Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ali Juma Mohamed (3 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia leo kupata nafasi ya kuchangia katika Wizara hii muhimu Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda sana nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi yote ya Ulinzi na Usalama Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyoanza vizuri kazi yake hii ya Urais wa Jamhuri ya Muungano, kwa kuliwezesha Jeshi letu la wananchi wa Tanzania pamoja na vyombo vingine vya ulinzi na usalama kuweza kufanya kazi zao kwa ueledi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini vilevile napenda nichukue fursa hii adhimu nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, kwa namna bora alivyowasilisha hotuba yake ya bajeti ya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. Pia napenda sana nimpongeze na kumshukuru sana Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi na Usalama Tanzania CDF, General Mabeyo pamoja na Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi Lieutenant General Yacoub Mohamed kwa namna bora wanavyoshirikiana na Mkuu wa Majeshi kwa kuweza kufanya kazi zao kwa ueledi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa vilevile napenda nilipongeze Jeshi letu kwa kuendelea kulinda mipaka yetu ya Tanzania na mpaka hivi sasa nchi yetu bado iko salama. Napenda nilipongeze Jeshi letu kwa kuendelea kuulinda Muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar na mpaka hivi sasa tumefikia umri wa miaka 57. Vilevile napenda nilishukuru Jeshi letu kwa kuendelea kuyaenzi na kuyalinda Mapinduzi Matukufu ya Zanzibar nayo pia yametimia umri wa miaka 57. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda nilipongeze jeshi letu kwa kuendelea kushiriki katika mission mbalimbali za Kimataifa hususani kule DRC Congo, Darfur Sudan pamoja na Lebanon. Vilevile napenda nilipongeze jeshi letu kwa namna bora wanavyoshirikiana na wananchi wa Tanzania, hasa pale panapotokea majanga na shida mbalimbali za wananchi, wanajitokeza na kuweza kusaidia jamii ya Watanzania na hii inaonesha wazi kuwa jeshi letu ni jeshi la wananchi kweli, ni jeshi la wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu nilikuwa napenda sana nijielekeze katika mashirikiano kati ya Jeshi la Kujenga Taifa na Jeshi la Kujenga Uchumi Zanzibar. Katika Ilani yetu ya uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ukurasa wa 157, chama chetu kimetuelekeza kushirikiana kati ya majeshi haya mawili ambayo yana dhamana ya ulinzi, lakini vilevile yana dhamana ya kukuza uchumi wetu wa pande zote mbili. Nilikuwa naomba sana ushirikiano huu uendelee vizuri japokuwa tayari umeshaanza katika kipindi kirefu, lakini nilikuwa naomba sana ushirikiano kati ya JKT na JKU kama yalivyozungumzwa katika Ilani yetu ya Uchaguzi yaendelee ili kuwapa nguvu vijana wetu wa pande zote mbili za Muungano ili kuweza kupata sifa zile za kuweza kujiajiri na kupata sifa za kuweza kuajiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa hivi Taifa letu lina vijana wengi ambao hawana kazi, lakini wengi wanategemea wapate ujuzi kupitia majeshi yetu haya mawili. Kwa hiyo, nilikuwa naomba sana kwa upande wa JKU tangu kuasisiwa kwake jeshi hili limekuwa likijihusisha sana na masuala ya kilimo, ufugaji, viwanda vya samani pamoja na michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba sana kupitia viongozi wa Jeshi la Kujenga Taifa – JKT waweze kushirikiana vizuri na JKU ili kuweza kuwapa nguvu nao kuweza kupata nguvu zaidi za kuweza kushiriki katika mambo mbalimbali ya Taifa letu na kuweza kukuza uchumi wetu wa Tanzania na katika hili tayari viongozi wetu wameshaonesha nia njema, hivi karibuni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, amewateua baadhi ya viongozi au Maafisa Wakuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania kwenda Zanzibar kwenda Wakuu wa Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mategemeo yetu uteuzi huu utaweza kaleta tija katika vikosi vyetu hivi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar pamoja na ushirikiano ya Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania pamoja na vikosi vyote vingine ambavyo kwa mujibu wa katiba yetu ni majeshi ya akiba. (Makofi)

Vilevile nilikuwa napenda nilikumbushe Jeshi letu pamoja na Waziri wa Ulinzi kuweza kuongeza nguvu katika ujenzi wa nyumba za askari wetu. Wenzangu wengi wamechangia suala hili, lakini la umuhimu jitihada zimefanyika, lakini naomba pia ziendelee kufanyika ili wanajeshi wetu waweze kuishi katika nyumba bora na kuweza kufanya kazi zao kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana nimuombe Mheshimwia Waziri aendelee na wazo hili la kuweka bima ya afya kwa ajili ya askari wetu pamoja na familia zao. Zoezi limeanza lakini nilikuwa naomba liende kwa haraka ili wanajeshi wetu waweze kufaidika na kupata hamu kubwa ya kuweza kufanya kazi za ulinzi na usalama katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Shaurimoyo naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuweza kunijalia kupata nafasi hii ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwa dhati kabisa nilikuwa napenda sana nimshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa kuweza kuwasilisha vizuri hotuba yake ya bajeti ya Wizara hii muhimu sana kwa Taifa letu, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile napenda nimpongeze Mkuu wa Majeshi (CDF) Jenerali Mabeyo, kwa kazi nzuri anayoifanya kupitia Jeshi letu hili, Jeshi la Ulinzi la wananchi wa Tanzania. Vilevile napenda nimpongeze kwa dhati Mnadhimu Mkuu wa Jeshi naye kwa kuendelea kufanya kazi nzuri kwa ajili ya Taifa letu na jeshi letu hili la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda vilevile kumpongeza Mwenyekiti wetu wa Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama, kaka yangu Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, amekuwa ni kiongiozi mwadilifu na anayetoa miongozo mizuri katika Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesimama hapa kwa ajili ya kulipongeza zaidi jeshi letu, Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. Katika kipindi kirefu katika nchi yetu wananchi wengi walikuwa wanachukua dhana ya kuwa jeshi letu kazi yake ni kulinda nchi pamoja na mipaka yake, lakini hivi sasa Jeshi letu la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania limejikita zaidi katika kuinua na kuimarisha uchumi wa Taifa letu na katika haya tumeona, Kamati tumetembelea mambo mengi na kiukweli tumeridhika na namna Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania wanavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jeshi letu sasa limekuwa lina taswira nzuri katika jamii yetu hasa katika mambo yale ya ujenzi majengo tofauti tofauti katika nchi yetu. Tumejionea majengo makubwa likiwemo la Ikulu ya Chamwino, Makao Makuu ya Ulinzi wa Taifa na Makao Makuu ya Idara ya Uhamiaji; haya ni majengo makubwa yamejengwa na wanajeshi wetu wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivi sasa katika nchi yetu ukitaka kuona majengo makubwa na mazuri, basi uangalie majengo ambayo yamejengwa na Jeshi la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukitaka kupata huduma nzuri za afya, basi angalia Jeshi la Wananchi wa Tanzania; ukitaka kuona mashamba mazuri ya kilimo pamoja na ufugaji wa samaki na mifugo mingine, basi liangalie Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania; ukitaka kuona elimu, shule ambazo zinasomesha vizuri, basi ni shule ambazo zinamilikiwa na Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania; ukitaka kuona wanamichezo wazuri, basi vilevile uangalie Wanajeshi wa Jeshi la Ulinzi wa Wananchi wa Tanzania; na hata ukitaka kuona burudani na mambo mengine mazuri, basi pia uangalie Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini vilevile jeshi letu limeikuza nchi yetu…

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ali kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jesca Msambatavangu.

T A A R I F A

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ukitaka pia kuona afya nzuri ya akili liangalie jeshi letu, ahsante. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Ali Juma Mohamed, Taarifa hiyo.

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, nimeipokea Taarifa ya dada yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jeshi letu vilevile limeipaisha vizuri nchi yetu ya Tanzania kwenye kada ya diplomasia ya nje. Jeshi letu mara kwa mara limekuwa likishiriki katika mission mbalimbali za kimataifa na hii imeipa taswira nzuri nchi yetu ya Tanzania ya kuonekana ni nchi ambayo inajitolea kwa ajili ya mataifa mengine duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya yote ambayo nimeyazungumza yamekuja kutokana na usimamizi mkuu wa Amiri Jeshi Mkuu kwa Majeshi ya Ulinzi na Usalama, mama yetu Samia Suluhu Hassan. Yeye ndiye ambaye anatoa miongozo mizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kumalizia katika nchi yetu kuna scheme nyingi za umwagiliaji ambazo zimetelekezwa. Kwa vile jeshi letu linafanya kazi vizuri, hasa kupitia SUMA-JKT, nilikuwa naomba hizi scheme zote za umwagiliaji ambazo zimetelekezwa basi wapatiwe JKT ili waweze kuziendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo machache, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kuweza kupata nafasi hii ya kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Awali ya yote napenda nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Katibu Mkuu na Naibu Katibu Mkuu, lakini vilevile napenda nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Mwinyi. Nawapa pongezi hizo kwa kuweza kushirikana kwa pamoja kuipaisha nchi yetu ya Tanzania katika anga ya kimataifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuzungumza suala hili la namna Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anavyofanya kazi kwa ajili ya kuipaisha nchi yetu katika anga ya kimataifa na hapa nataka nizungumzie kuhusu hii Royal Tour pamoja na Dubai Expo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Watanzania wenzetu wachache wamekuwa wakitumia mitandao ya kijamii katika kubeza hili suala la filamu hii ya Royal Tour, lakini nafiriki wangekuwa wanaijua faida yake nafikiri wangetulia kwa sababu na wao siku yoyote kama si leo kesho itawagusa katika mzunguko wa uchumi wetu wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, filamu hii la Royal Tour inaweza ikaongeza idadi kubwa ya wageni ambao wataingia nchini hususani watalii, lakini vilevile tunategemea kupata wawekezaji wengi kutoka mataifa mbalimbali kuja kuwekeza katika nchi yetu ya Tanzania na wanapokuwa wengi maana yake malipo ya viza yatakuwa mengi maana yake tutapata pato kubwa, lakini hoteli zetu zitajaa na zitachukua watalii kwa madaraja yote daraja la juu daraja la chini na madaraja ya kati, lakini vilevile italeta ongezeko kubwa la fedha za kigeni na hii itasababisha kuwa uchumi wetu wa Tanzania kuwa upo juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ukurasa 182 Ilani yetu imeelezea namna fursa ambazo zinatakiwa zifanywe na viongozi wetu kuweza kuhangaika na kuweza kuwatafutia maisha mazuri wananchi wote wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, historia inatuambia muasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Kambarage Nyerere alitumia nafasi yake ya Urais muda mwingi kwa ajili ya kuweka mahusiano mazuri ya Tanzania na mataifa mbalimbali duniani, kwa hivyo haya ambayo anayafanya Rais wa sasa wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan sio mambo mageni yeye amejielekeza zaidi sasa hivi katika diplomasia ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nilikuwa napenda niwapongeze Mabalozi wetu hususani Balozi Mavura ambaye anaiwakilisha Tanzania katika nchi ya South Korea, amekuwa na jitihada kubwa katika kuunganisha Watanzania ili kuweza kupata fursa mbalimbali ambazo zipo South Korea. Lakini vilevile nimpongeze Balozi Kairuki ambaye analiwakilisha Taifa letu katika nchi ya China naye amekuwa mstari wa mbele katika kuhangaika na kuweza kuleta fursa mbalimbali katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Balozi Mahmoud Thabit Kombo ambaye anaiwakilisha nchi yetu katika nchi ya Italy, naye amekuwa anafanya jitihada kubwa katika kuunganisha Watanzania na hivi karibuni kulikuwa kuna tamasha kubwa kule nchini Italy ambalo linaitwa Macfrut lilifanyika katika mji wa Rimini, Italy tamasha hili liliwapeleka wadau wengi wa kilimo wa nchi yetu ya Tanzania na banda la maonesho ambalo lilitumiwa na Watanzania lilikuwa ni kivutio kikubwa kwa bidhaa mbalimbali ambazo zilioneshwa pale. Hivi sasa tunajionea wazi kwa Taifa letu linaanza kuwabeba wakulima wa kawaida wa Tanzania na kuwapeleka katika soko la kimataifa huko ughaibuni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hili suala sio suala la kubeza kwa hiyo tunaomba tumuunge mkono Rais wetu pamoja na Mawaziri wote ambao wanafanya kazi kwa niaba yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kiasi cha miaka minne iliyopita nchi yetu ya Tanzania iliingia mkataba na nchi ya Qatar na mkataba huu ulionesha wazi kuwa namna ya kuweza kupata ajira kwa Watanzania vijana pamoja na Watanzania ambao wana kada mbalimbali za kitaalam. Sasa hivi ni mwaka wanne lakini inaonekana bado jitihada za kuchukua fursa hizo na kuzifanyia kazi bado zimezorota, kwa hiyo nilikuwa namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa, malizia, sekunde 10.

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Waziri akatapokuja hapa basi angalau aje kutueleza kuhusu mkataba huu wa Tanzania na nchi ya Qatar.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo machache naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)