Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Ummy Hamisi Nderiananga (5 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI WA WAZIRI MKUU (WATU WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kuniwezesha leo hii kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu. Vile vile niwatakie mfungo mwema wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhan Waislam wote duniani na katika Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. John Pombe Magufuli pamoja na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuweza kuniamini ili niwatumikie Watanzania katika nafasi hii ya Naibu Waziri, Watu Wenye Ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda vile vile niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuendelea kuamini katika uwezo wangu na kuweza kunibakiza ili niweze kutumikia watu wenye ulemavu, Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile kwakuwa sisi ni watu wenye ulemavu, napenda niendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwateua wenzangu wenye ulemavu kuwa Makatibu Wakuu na Manaibu Katibu Wakuu na katika maeneo mengine. Tunamhakikishia tutaendelea kuchapa kazi kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niende kujibu maswali ambayo yaliulizwa, mojawapo likiwa ni suala la Vyama vya Watu Wenye Ulemavu na kutatua migogoro yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nipende kulihakikishia Bunge lako Tukufu kwamba tumetambua vyama 14 vya watu wenye ulemavu wa aina tofauti na tunaendelea kufanya nao kazi kwa karibu kuhakikisha kwamba migogoro haipo.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumefanya chaguzi na tumevisimamia vyama hivi viweze kuiendesha vizuri. Hali kadhalika nimefanya ziara katika mikoa takribani tisa ambapo nimefanya vikao vya kujengeana uwezo na viongozi wa vyama hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lipo pia swali liliulizwa na Kamati kuhusu Mfuko. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu ameshatoa maelekezo ya kuhusu Mfuko, tutaleta pia maelekezo ya ziada hapo ambapo tutakuwa tumepata utathmini utakaoturuhusu sasa kuzindua Mfuko wa Taifa wa Watu Wenye Ulemavu na tutawakaribisha pia wadau waweze kuchangia katika Mfuko huu ili tuweze kutoa huduma kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na suala la register ya watu wenye ulemavu na ni eneo ambalo tuliona ni la muhimu sana, kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa haraka sana tumefanya utambuzi wa watoto wenye ulemavu ambao mpaka sasa tumefanya utambuzi wa watoto 28,698 wenye ulemavu, ambao wengi wao walikuwa wamefichwa ndani na sasa wametolewa na tutahakikisha wanasoma kweli kweli.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuwepo kwa mwongozo wa utambuzi wa watu wenye ulemavu ambao ni register maalum sasa kwa wale ambao wana umri mkubwa wa ujana na kuendelea, tumeshatoa maelekezo kupitia TAMISEMI tarehe 8 Aprili, 2021 wameshateremshiwa viongozi ili wayafanyie kazi. Nitoe rai waendelee kukusanya takwimu hizo na nitakuwa nafuatilia kwa ukaribu sana katika eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vile vile suala la asilimia mbili kwa watu wenye ulemavu; baada ya kufanya tathmini ya kina na kuzunguka katika Mikoa hii niliyoitaja, ya Simiyu, Mara, Dar es Salaam, Kilimajaro na kadhalika. Tumepata maoni ya watu wenye ulemavu na tukaona kwa haraka sana sisi ndani ya Serikali tubadilishe pia kanuni. Hivyo, tumebadilisha kanuni na kwa sasa watu wenye ulemavu zile asilimia mbili zao wataweza kupata kwa mtu mmoja mmoja na wakitaka kikundi mwisho ni watu wawili, wakitaka zaidi sawa, lakini kikubwa sisi tunatii kiu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye hili tutaendelea kujipima kuona namna ambavyo fedha hizi zinakuwa na ufanisi. Mimi binafsi nitoe rai watu wenye ulemavu wapewe fedha ambazo zinaweza kuwaletea matokeo badala ya kupewa fedha kidogo kidogo, wasaidiwe kupata miradi ambayo ni mizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la ajira, mwezi Januari na Februari tuliajiri Walimu 243 wenye ulemavu. Vilevile upande wa Internship tumeingiza Walimu 100. Niseme kwamba, tutaendelea kusimamia upande wa Serikali ajira zote zinazotoka, kipaumbele kiwe ni kwa watu wenye ulemavu na tutawaingiza kwa wingi na kwa kadri ambavyo ajira hizo zitatolewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa taasisi binafsi na mashirika kuendelea kuajiri na kuwaamini watu wenye ulemavu kama sisi ambavyo tumeaminiwa hapa na tunafanya kazi hii nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la unyanyapaa na ubaguzi dhidi ya watu wenye ulemavu hususan kwenye eneo la elimu, liliulizwa swali hili. Napenda niseme kwamba, Serikali tunaweka mkazo sana katika kuhakikisha wanafunzi wenye ulemavu wanapata elimu. Kwa mwaka huu wa fedha 2020/2021 tumeshanunua vifaa saidizi 51,339 na tumevigawa katika shule za msingi na sekondari na tutaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa ni suala hili la unyanyapaa na ubaguzi. Tutaendelea kufanya kaguzi za mara kwa mara kuhakikisha hakuna mtu anayewanyanyapaa na kuwatumikisha watu wenye ulemavu kama tukio lililotokea Dar es Salaam. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima na afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa kuniamini na kuniteua ili niwe Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu ninayeshughulikia Sera, Bunge na Uratibu. Namhakikishia Mheshimiwa Rais Samia kwamba sitamwangusha na kazi iendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nitumie fursa hii pia kuwashukuru sana Kamati yetu chini ya Mheshimiwa Mwenyekiti, Fatma Toufiq na Wajumbe, kwa kazi kubwa na nzuri wanayofanya ya kuishauri Serikali katika mapambano dhidi ya Virusi Vya UKIMWI na dawa za kulevya nchini. Niseme kwamba ushauri walioutoa sisi kama Serikali tumeupokea, tutaufanyia kazi na tutaleta maendeleo ya yale tuliyofanyia kazi katika Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la kuhamasisha wanaume kupima, naomba niseme kwamba Serikali imeendelea na mkakati wa kuwahamasisha wanaume kupima VVU na kujua afya zao. Tuna Mkakati unaitwa Male Engagement Strategy. Kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa Majaliwa, kwa kukubali kuwa balozi wa kuhamasisha wanaume kupima Virusi Vya UKIMWI. Kazi hiyo imeendelea vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kadri tulivyokuwa tunakwenda mbele tukaona tuboreshe programu hii na kuhakikisha kwamba tumeanzisha plan nyingine ambayo inaitwa Male Involvement Culture Plan ambayo itawajumuisha sasa watu wengi; wanawake, viongozi wa dini, watu ambao ni maarufu katika maeneo yetu kuhakikisha kwamba wanashirikiana na wanaume kuwahamasisha. Nitumie fursa hii kuwahamasisha wanaume mliopo humu Bungeni na ninyi kumuunga mkono Mheshimiwa Waziri Mkuu ili kupima afya zenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika programu ya vijana Kamati imetushauri vizuri sana na tunawashukuru sana Kamati kwa kutambua na kuona kwamba eneo hili la vijana linatakiwa kupewa mkazo wa hali ya juu. Nipende kuwaambia vijana wote nchini Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na Serikali nzima tunawathamini na tunawapenda sana vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata mimi kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu nilizindua programu maalum ya vijana kwenye redio na tv inaitwa Ongea Programme ipo katika East Africa Radio na Clouds Media tunashirikiana nao pia na mtandao wa Instagram kuhakikisha tunatoa elimu kwa vijana wetu na tutaendelea kuhakikisha kwamba tunawafikia vijana wengi zaidi na zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwatoe wasiwasi; kazi inaendelea vizuri, Ofisi ya Waziri Mkuu tumejipanga vizuri na maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge tumeyachukua na tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kuwa miongoni mwa viongozi wenye ushawishi mkubwa Duniani na kupewa Tuzo ya mafanikio ya ujenzi wa miundombinu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, nilishukuru sana Bunge lako Tukufu kwa kupitisha azimio hili la kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Serikali napenda nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Wabunge waliotangulia wamesema, nami niseme kwa lugha ya wenzetu, a leader is the one who lead the way and show the way. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ameyaonesha kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirejee kipindi fulani nchi ya Marekani walipokumbwa na anguko la uchumi, walimpata Rais Franklin Roosevelt. Rais huyu aliwaonesha namna ya kufufua uchumi wa Marekani, akawaambia kwamba I will show you the new deal. Mheshimiwa Rais Samia ameichukua nchi kipindi ambacho tupo katika janga kubwa la corona. Uchumi wetu umeanguka lakini Mheshimiwa Rais Samia ametuonesha njia, tumepanda kwenye uchumi wetu uliokuwa umeanguka kwa asilimia nne, sasa tuko 5.2 na dhamira yake ni kuupeleka kurudi kwenye 6.8. Nani kama Rais Samia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais Samia Saluhu tuzo hii aliyopewa ni ya heshima kwake, kwa Watanzania, kwa wanawake na dunia. Nchi yetu tunajivunia sana kwa uwepo wa Rais Samia Suluhu Hassan kwa sababu kwa kazi zake nyingi na kubwa alizozifanya Waheshimiwa Wabunge wamezieleza hapa, Mheshimiwa Rais kwenye elimu amefanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaalike pia wanaoendelea kutoa tuzo duniani kwenye elimu wamwone Mheshimiwa Rais Samia, kwenye afya wakitaka kutoa tunaye jemedali mpambanaji Mheshimiwa Rais Samia ambaye amefanya kazi kubwa na nzuri sana ya kuhakikisha kwamba Watanzania wanapata maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais Samia toka amepewa kazi ya Urais halali, anachapa kazi usiku na mchana, Watanzania tumemwona, tumefurahia kazi yake, amefanya kazi kubwa sana kwenye royal tour na watalii wameanza kuja na kuiunga mkono Serikali yetu. Kwa kweli sisi sote tumefurahi tumefarijika sana kwa tuzo hii ya heshima kwa Mheshimiwa Rais, tunamwombea kwa Mwenyezi aendelee kumlinda, ambariki kwenye majukumu yake ili aweze kuendelea kuwaletea Watanzania maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaendelea kumuunga mkono Mheshimiwa Rais Samia, tunamwambia kazi iendelee na sisi tunaoamini katika uongozi wa hoja na kazi, tunasema kazi yake inaendelea vizuri, hongera sana kwa Mama, Mungu ambariki sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA NA VIJANA (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ninamshukuru kipekee Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kutujalia afya njema na kuweza kukutana katika Bunge hili. Nitumie fursa hii kuwatakia heri ya mwezi Mtukufu wa Ramadhani Waislam wote katika Taifa letu na dunia nzima na niwatakie heri ya kwaresma Wakristo wote.

Mheshimiwa Spika, vilevile nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassani kwa kutimiza mwaka mmoja wa kuchapa kazi kwa weledi na bidi, hongera sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa uniruhusu niende katika hoja za Kamati zetu zote mbili zimeshauri vizuri, na ninawashukuru pia Waheshimiwa Wabunge kwa michango mizuri ambayo mmetupatia ili kuboresha eneo letu la bajeti Ofisi ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba fedha za maendeleo zilizotengwa Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya mwitiko wa masuala ya UKIMWI Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Samia tutazitoa fedha zote hizo ndani ya mwezi huu wa Aprili katika robo ya nne hii. Kwa hiyo niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kazi inaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la fedha za ndani kwa ajili ya mapambano dhidi ya virus vya UKIMWI, niwaambie tu kwamba Serikali imeongeza fedha kutoka kiasi cha Shilingi Bilioni Moja mwaka 2021/2022 na katika bajeti hii ya leo ambayo mtatupitishia Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mheshimiwa Rais Samia tumeongeza fedha kwa asilimia 88 na sasa zitakuwa ni Shilingi Bilioni Moja Milioni Mia Nane na Themanini katika mapambano dhidi ya virus vya UKIMWI na kazi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, lipo suala liliongelewa kuhusu mfuko wa mapambano dhidi ya virus vya UKIMWI, tumepokea maoni na ushauri wa Kamati yetu ya masuala ya UKIMWI na kwa uharaka sana mwezi wa pili mwaka huu tumesaini mkataba na taasisi ya sekta binafsi ili kuona namna ambavyo tunaweza tukatafuta fund ndani yetu tuka-mobilize resource. Kwa hiyo, niwaambie Watanzania kwamba kazi hiyo inaendelea na niwashukuru sana taasisi ya sekta binafsi Tanzania kwa kutukubalia ombi letu la kuingia nao makubaliano hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni chanzo cha mapato ya mfuko wa ATF, tumefanya marekebisho ya sheria katika kifungu cha 16 cha Sheria ya Kodi ya Mapato Sura Na. 332 ya mwaka 2020 ambayo hii inaleta nafuu kwa watu watakaochangia mfuko wa ATF.

Mheshimiwa Spika, kwa hili niwakaribishe sana Ofisi ya Waziri Mkuu, muungane na Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia kuchangia kwa sababu unapochangia unapata nafuu ya kodi. Niwapongeze pia kampuni kama ya Barrick ambayo wameweza kutupatia fedha kwa kupitia kipengele hiki na wao wamepata nafuu ya kodi kwa hiyo niyakaribishe makampuni mengine yote kuja kuiunga mkono Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ni suala la udhibiti wa dawa za kulevya. Serikali ya CCM chini ya Mheshimiwa Rais Samia tunaendelea na mapambano dhidi ya madawa ya kulevya. Mamlaka za kudhibiti dawa za kulevya iko imara sana na kazi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Julai, 2021 hadi Februari, 2022 tumefanya operation mbalimbali kupitia mamlaka ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya na tumekamata watuhumiwa takribani 11, 716 wa dawa za kulevya za kilogram 35,226 wa dawa ya kulevya.

Mheshimiwa Spika, vilevile tumeteketeza ekari 185 za mashamba ya bangi na ekari 10 za mashamba ya mirungi kuanzia kipindi hiko niwahakikishie Watanzania kwamba kazi ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya inaendelea na Serikali iko imara.

Mheshimiwa Spika, lipo jambo Waheshimiwa Wabunge walitushauri kwamba tufundishe elimu hii ya athari za dawa za kulevya, niwaambie tumeingia makubaliano ya Wizara ya Elimu na taasisi zingine tayari tumeshaanda mwongozo wa namna ya kufundisha.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo niwashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Usimamizi wa Maafa, 2022
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU (MHE. UMMY H. NDERIANANGA): Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na Mheshimiwa Waziri na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge waliompongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuridhia tulete Muswada huu wa Sheria katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile niwashukuru na kuwapongeza sana Wajumbe wa Kamati yetu ya Katiba na Sheria wakiongozwa na Mwenyekiti Dkt. Mhagama kwa kazi nzuri na kubwa waliyofanya ya kutushauri sisi Serikali mpaka tukafika hapa tulipofika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimpongeze kipekee Mheshimiwa Waziri wetu wa Nchi, Mheshimiwa George Simbachawene kwa uongozi mahiri alioonesha na kuweza kutusadia kufika katika hatua hii pamoja na Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na watushi wote wa Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wametoa maoni yao na sisi kama Serikali tunawashukuru sana na tunawapongeza kwa michango mizuri yenye kuleta mwelekeo wa kuboresha shughuli tuliyoifanya. Hata hivyo, niseme katika baadhi ya maeneo tumeshauriwa kuendelea kutoa elimu ya usimamizi wa maafa. Tunalichukua jambo hili, tutaendelea kutoa elimu ya usimamizi wa maafa na niwaombe Waheshimiwa Wabunge tuungane mkono tupitishe sheria hii ili kazi iweze kuanza mara moja.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili tutaendelea kutumia vyombo vya habari na majukwaa mbalimbali kuendelea kutoa elimu hii, lakini ushauri wa kupeleka elimu katika shule, vyuo na maeneo mbalimbali tumezingatia.

Mheshimiwa Spika, tunatambua suala la maafa ni suala mtambuka kama lilivyoelezwa na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliozungumza hapa, linahitaji ushirikiano wa kila mmoja na nilipokuwa naandika maoni hapa nilikuwa nafurahi kwamba kwa pamoja sisi wawakilishi wa wananchi tumeonesha mwitikio, kila mtu amelichangia na hata tulipokuwa tunaendelea kuchangia Muswada huu tumeendelea kutoa elimu kwa umma. Watanzania waliotuona wamesikia na wamefahamu kuhusu suala la maafa.

Mheshimiwa Spika, ipo hoja hapa ya kuwa na mlolongo wa kamati, kamati hizi ni kubwa na kuna posho. Nataka niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge na Watanzania, hakuna posho yoyote kamati hizi zitaketi kwa mujibu wa majukumu yao. Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya anapoenda kwenye kamati yupo kazini, Mkurugenzi yupo kazini, kwa hiyo hakuna namna ambayo kutakuwa kuna posho au fedha nyingi zitatumika kwa ajili ya kuketi tu vikao, fedha nyingi zitaenda kwa ajili ya kushughulikia kazi ya maafa.

Mheshimiwa Spika, kuna jambo hapa kidogo kama linatatiza hivi kwenye suala hili la maafa. Katika kujenga uelewa wa pamoja tunaposema usimamizi wa maafa inajumuisha kujiandaa kukabiliana na maafa kabla hayajatokea, wakati maafa yametokea na kurejesha hali baada ya maafa kutokea. Kwa hiyo huu mzingo mzima wa usimamizi wa maafa, hapa ndio sheria hii inatupa namna nzuri zaidi ya kusimamia eneo hili la maafa.

Mheshimiwa Spika, mwisho, tutaendelea kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi katika kukabiliana na maafa na nilipe taarifa Bunge lako Tukufu kipindi ambako bado hatujakutana hapa wenzetu wa Shirika la WFP wameendelea kutu-support Serikali na walitupatia vifaa.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa tunavyo vifaa ambavyo ni drowns, pakitokea maafa pengine Dodoma Mjini tuna uwezo wa kurusha drown dakika 45 imeshatuambia kwamba maafa haya yamesambaa kwa kiasi gani. Kwa hiyo na sisi tunaenda kwenye usasa, hatukai tena kizamani. Tutaendelea kushirikiana na wadau wa ndani na nje ya nchi lakini na ukanda wetu wa SADC, Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa pamoja tushirikiane kwenye suala hili.

Mheshimiwa Spika, naomba tena kwa unyenyekevu mkubwa niwaombe Waheshimiwa Wabunge watuunge mkono, tupitishe Sheria hii ya Usimamizi wa Maafa ya Mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, niseme kwamba naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)