Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Prof. Kitila Alexander Mkumbo (29 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii na nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa maoni yao mazuri sana kuhusu Sekta ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijajibu baadhi ya hoja, naomba niseme mambo mawili ya kihistoria. Moja, naomba nichukue nafasi hii kukipongeza sana Chama cha Mapinduzi kwa kuadhimisha miaka 44 tangu kilipozaliwa na ukijumlisha na wazazi wake, miaka 60 leo mambo ambayo yanakifanya kuwa chama kikongwe kabisa Barani Afrika. Historia ya leo inakiweka Chama cha Mapinduzi kuwa chama ambacho kimekaa madarakani kwa muda mrefu kuliko vyama vyote Afrika. Mwaka juzi kulikuwa na chama ambacho kilikuwa kimekizidi sitaki kusema nchi gani lakini kimeondolewa madarakani kwa hiyo kimebaki Chama cha Mapinduzi na nakipongeza sana kwa historia hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, Bunge hili zimeshatolewa hotuba hapa za kufungua Bunge na hotuba za wakuu wa nchi zaidi ya 20 lakini zipo hotuba tano ambazo ni za kihistoria ikiwemo hizi hotuba mbili ambazo tunazijadili leo. Kwa ruhusa yako kwa haraka sana, hotuba ya kwanza ya kihistoria ambayo inajulikana katika nchi hii ndani ya Bunge hili ni hotuba ya Desemba, 1962 iliyotolewa na Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere. Hotuba hiyo ndiyo iliyozaa Jamhuri ya Tanganyika. Lengo lake kubwa ilikuwa ni kujenga Umoja wa Kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya pili ni ya tarehe 25 Aprili, 1964 iliyotolewa katika Bunge hili. Lengo la hotuba hiyo Mwalimu alitumia kuomba ridhaa ya Bunge kuridhia Mkataba wa Muungano kati ya Tanganyika na Zanzibar. Hotuba hiyo ndiyo iliyozaa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya tatu muhimu ya kihistoria katika nchi hii ya tarehe 29 Julai 1985. Hotuba hii aliitumia Mwalimu Nyerere kuaga…

WABUNGE FULANI: Uwekezaji.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS (UWEKEZAJI): Tulia wawekezaji unakuja. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya nne ni ya tarehe 20 Novemba, 2015 iliyotolewa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. Hotuba hii lengo lake kubwa ilikuwa ni kujenga msingi wa kupambana na ufisadi na kuimarisha maadili ya utumishi wa umma na matokeo yake wote tumeyaona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya tano ya kihistoria ni iliyotolewa tarehe 13 Novemba, 2020. Lengo lake kubwa ni kulinda na kuendeleza status ya nchi ya uchumi wa kati. Hotuba hii imetoa mwelekeo wa kiuchumi wa nchi na imejengwa katika uwekezaji kama njia ya kukuza uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nichukue hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kunipa nafasi kuwa sehemu ya Serikali yake ili kutekeleza maono makubwa ambayo yapo ndani ya hotuba hii ya tarehe 13 Novemba, 2020. Lengo kubwa ambalo Mheshimiwa Rais ametuelekeza na ambalo tunalisimamia kwa bidii na kwa maoni ambayo Waheshimiwa Wabunge wameyatoa ni mambo matatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tuhamasishe uwekezaji wa ndani nan je ya nchi. Katika kuhamasisha uwekezaji Waheshimiwa Wabunge wanairudia ile kauli ya Mheshimiwa Rais, tunapozungumzia uwekezaji sio lazima moja, iwe kutka nje, lakini sio lazima uwe bilionea. Unatumia nafasi yako ndogo uliyonayo unaweka akiba, unapata mtaji, unawekeza unajenga uchumi, unaanza kujitengenezea mazingira kutoka kuwa elfunea kwenda milionea na hatimaye kuwa bilionea. Kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge ambao ni Wajumbe wa Mabaraza ya Madiwani waende kuhamasisha katika halmashauri zao ili halmashauri zetu zitengeneze mazingira ya uwekezaji, ikiwemo kutenga maeneo ya uwekezajikwa wawekezaji wetu wa ndani, lakini pia wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tumepewa kazi ya kuwezesha wawekezaji ndani ya nchi waliokwisha kuwekesha hapa kwa sababu, balozi mkubwa sana uwekezaji ni yule muwekezaji ambaye tayari yupo ndani ya nchi. Kwa hiyo, naomba sana Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha halmashauri zetu ili ziweke mazingira mazuri ya kuhudumia wawekezaji ambao wapo. Pale ambapo kuna changamoto za wawekezaji tuzishughulikie kisheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho katika uwekezaji, ni muhimu sana kuwahudumia. Kwamba, pale ambapo mwekezaji ameshaweka, amewezeshwa, kiwanda kipo pale, ni muhimu sana mamlaka zilizopo kuanzia ngazi ya halmashauri wawekezaji hawa wahudumiwe kwa kupatiwa mahitaji muhimu. Tunafanya mawasiliano ya karibu na wenzetu katika Wizara mbalimbali ili kuhakikisha kwamba, huduma muhimu zikiwemo umeme, maji na barabara zinapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli, kwa sasa katika nchi yetu huduma za msingi za kufanya uwekezaji mkubwa zipo vizuri ikiwemo katika eneo la miundombinu. Kama ni barabara maeneo yote makubwa yameshaunganishwa kwa mtandao wa barabara za lami. Kama ni usafiri wa majini karibu maziwa yetu yote makubwa ikiwemo na bahari tayari kuna vyombo vya usafiri vya kutosha, lakini pia usafiri wa anga umeimarika sana. Kama ni hali ya kisiasa ambayo ni ya msingi sana katika uwekezaji Tanzania ndio inaongoza kwa utulivu wa kisiasa Afrika. Kwa hiyo kwa kweli Waheshimiwa Wabunge tuendelee kuhamasisha wawekezaji waje. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, tupo katika mchakato wa kuifanyia mabadiliko Sheria ya Uwekezaji ili kuiboresha zaidi ikiwemo kuimarisha taasisi yetu ya TIC ambayo Waheshimiwa Wabunge wengi wametoa maoni mazuri namna ya kuiboresha. Pia tunatengeneza mkakati wa kuhamasisha uwekezaji katika ngazi ya kitaifa, lakini pia katika ngazi ya mkoa hadi katika ngazi ya halmashauri na ndio maana tumekuwa tukipita Mheshimiwa Waziri Mkuu akituongoza kwenda kuzindua Miongozo ya Uwekezaji katika ngazi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue nafasi hii kuwaalika sana Waheshimiwa Wabunge katika mikoa yenu. Pale ambapo tumekuja kuhamasisha na kuzindua miongozo hii naombeni sana mshiriki. Niwapongeze sana Mkoa wa Iringa, tulikuwa huko juzi, imefanyika kazi kubwa na nadhani mikoa mingi inaendelea kuzindua na hivi karibuni tutakwenda kuzindua katika mikoa mingine chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, tumeaswa kila unapopata nafasi ushukuru watu ambao wamefanya tofauti katika maisha yako. Sasa nataka nichukue nafasi hii kwanza kukishukuru sana Chama Cha Mapinduzi kwa fursa kilichonipa ya kugombea nafasi ya ubunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashukuru sana wananchi wenzangu wa Jimbo la Ubungo kwa kunipa nafasi ya kuwa Mbunge wao, hatimaye tukakomboa Jimbo la Ubungo lililokaa Misri kwa miaka 10 sasa lipo Kaanan, tumetoka Misri sasa tupo Kaanan. Niwapongeze sana, tutashirikiana sana kuhakikisha kwamba, mambo ambayo tumeyaahidi tunayafanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Viwanda Na Bishara
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge ambazo wamezitoa katika hoja yangu niliyowasilisha asubuhi.

Kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru sana wewe mwenyewe kwa jinsi ambavyo umeweza kuongoza mjadala huu vizuri sana na kuweza kuniongoza pia katika uwasilishaji wangu. Niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri sana katika kuboresha hoja yangu. Lakini kwa nia njema ya kuendeleza Sekta ya Viwanda na Biashara.

Nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kujibu vizuri sana baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge ambazo wamezitoa hapa. Tumepokea michango mingi, michango 20 ya kuchangiwa hapa moja kwa moja na michango miwili kwa njia ya maandishi. Niwaahidi tu kwamba…

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge waliochangia kwa maandishi naambiwa wako kumi, niwaahidi Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa kauli na kwa maandishi tutajibu hoja zote hizi bila kuacha hoja hata moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, naomba tu kusema kwamba hoja zote ambazo zimetolewa ni za msingi. Zile ambazo ni ushauri, tunazipokea na tutazifanyia kazi zaidi katika kuboresha utendaji wa kazi kama Wizara. Yale ambayo yanahitaji uboreshaji wa kisheria na kimiongozo, tutayafanyia kazi. Baada ya kusema hayo, naomba uniruhusu nipitie baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, nianze na hoja inayohusu miradi ya makaa ya mawe wa Mchuchuma na chuma cha Liganga. Kama mnavyofahamu, wote tumepitisha Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano hivi karibuni katika Bunge hili hili. Mradi huu ni moja ya miradi 17 ya miradi ya kielelezo ambayo Serikali imepanga kuitekeleza. Ni mradi ambao unaendelea. Ulikuwepo katika Mpango wa Maendeleo uliopita na Waheshimiwa wengi wamehoji kwa nini mradi huu umechelewa. Kwa kweli umechelewa, Serikali haipingi hilo, lakini muhimu ni kujibu hasa kwanini umechelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tukubaliane katika hatua ya utekelezaji ya miradi mikubwa kama hii kuna hatua nyingi, tunafahamu feasibility study ya mradi huu ilikamilika mwaka 2012, ni kwa feasibility study hii ndiyo tukagundua kwamba tunazo tani milioni 428 za makaa ya mawe katika eneo la Mchuchuma na tunazo tani milioni 126 za chuma katika eneo la Liganga. Hiyo ilikuwa ni hatua ya kwanza ya feasibility study. Lakini baadaye, ikaja ikagundulika kwamba pale sio tu kwamba tuna mawe na chuma, tunayo pia madini ya maana sana duniani, madini ya titanium na vanadium.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maandalizi ya mradi pia kama Waheshimiwa Wabunge walivyoeleza, upo ujenzi wa barabara, kilometa 221 pamoja na ujenzi wa reli. Hii nayo ni hatua muhimu. Lakini hatua ya tatu ni kufanya tathmini ya mazingira; athari za mazingira katika utekelezaji wa mradi huo, hili limefanyika. Kwa hiyo, kusema kwamba hakuna kitu ambacho kimefanyika sio sahihi. Yapo mambo ambayo yamefanyika na kwa kweli, zile shughuli za msingi za Serikali imezifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya nne ambayo ni ya msingi ilikuwa ni kutafuta mwekezaji. Mradi huu investment cost yake ni zaidi ya dola milioni tatu. Kwa hiyo, ni mradi ambao ilikuwa lazima kutafuta mwekezaji ili kushirikiana na Serikali kupitia Shirika la NDC kuweza kutekeleza. Kwa unyeti wa mradi wenyewe na ukubwa wa mradi wenyewe, kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge wameeleza, ni mradi muhimu sana kwa maendeleo ya nchi hii. Ni mradi ambao unabeba rasilimali za msingi na muhimu za Taifa. Kwa hiyo, lazima Serikali yoyote duniani na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ingetaka kujiridhisha kuhusu faida ambazo Serikali na nchi hii itazipata sio tu leo. Miaka mingi ijayo, unazungumzia tani milioni 428 za makaa ya mawe na tani milioni 126 za chuma. Unazungumzia uwepo wa madini ya titanium and vanadium, some of the most precious minerals in the world. (Makofi)

Kwa hiyo, ni mradi ambao lazima ujiridhishe; mwekezaji akapatikana, tukafanya majadiliano, lakini hatukufikia mwisho kwa sababu mwekezaji alitaka masharti ambayo hayakubaliki kwa nchi, kwa sababu mengi ya masharti yanapingana na sheria zetu, hasa sheria ambazo Waheshimiwa Wabunge tumezipitisha hivi karibuni za mwaka 2017.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mazingira hayo ingekuwa ni vigumu Serikali kusema aah, twende tuanze kutekeleza mradi. Bahati nzuri mwekezaji anaelekea kukubali masharti mengi ya Serikali na taarifa ambazo ninazo kutoka kwa Government Negotiating Team, bahati mbaya ni kwamba wawekezaji wameshindwa kuja kwa sababu ya mazingira ya sasa ya pandemic, lakini mazungumzo yanarudi na masharti mengi anaelekea kukubaliana na akishakubali masharti ya Serikali ambayo tunajiridhisha kwamba ni muhimu kulinda maslahi ya nchi, mradi utaanza kutekelezwa ili mradi uwe na manufaa, sio tu kwa kizazi cha leo sisi hapa, lakini kwa miaka mingi ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, isije pakatokea hapa wakataka kutafuta hili Bunge la Kumi na Mbili waliokuwepo ni akina nani ambao walikwenda kuiuza nchi? Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge Serikali inatambua umuhimu wa mradi huu kama ambavyo nyie mnatambua na Serikali ipo committed kuutekeleza na ndio maana upo katika documents zetu zote za ajenda za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja nyingine ambayo ningetaka kuitolea maelezo ni suala la blueprint. Waheshimiwa Wabunge wameongea kwa uchungu kuhusu blueprint. Kwanza niwakumbushe, blueprint tumeipitisha kama nchi tarehe 01 Julai, 2019, maandalizi yakaanza katika mwaka 2019/2020, mwaka 2020/2021 tukafanya mambo ya kawaida yakiwemo kuondoa baadhi ya tozo, ada na adhabu ambazo zilikuwa zinakwaza biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukatengeneza taasisi za utekelezaji wa blueprint. Tukasema tutengeneze action plan, tukatengeneza action plan imekamilika na action plan hii ukiisoma inaanza utekelezaji wake rasmi mwaka 2021/2022 na ndio maana moja ya kitu ambacho tumepata, tumepata Euro milioni 11.5 kutoka Jumuiya ya Ulaya kwa ajili ya kutekeleza mradi huu. Na moja ya hatua kubwa sana ni kwamba, tunakwenda kufungua One Stop Centres kwenye kila Halmashauri, kwa sababu tathmini inaonesha kwamba, tumefanya mengi katika ngazi ya kitaifa, Serikali Kuu, lakini kwenye local government wanaendelea ku-behave business as usual.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio likaandikwa andiko, tumepata fedha Euro milioni 11.5 zaidi ya shilingi bilioni 50, hizi zote zinakwenda kwenye ngazi ya local government. Moja ya kazi ya kufanya ni kutengeneza ki-TIC kingine kule ambacho kitakuwa na One Stop Centre ili mwekezaji akienda apate huduma zote palepale haraka iwezekanavyo, kwa hiyo, ni hatua kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunaendelea na maboresho ya sheria na baadhi ya sheria Waheshimiwa Wabunge mmezipitisha wenyewe hapa ikiwemo Arbitration Act ambayo imepita mwaka jana. Hii inakuwa ni moja ya utekelezaji wa blueprint, lakini mwaka huu tunafanya marejeo ya sheria kadhaa ambazo zitakuja hapa Bungeni kupitia Miscellaneous Amendment na zingine kama ni sheria za kawaida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumefanya mazungumzo na Ofisi ya Waziri Mkuu kuhusu suala zima la work permit ambalo mmelizungumza hapa. Hili nalo tunalifanyia kazi, yale maeneo ambayo yanahitaji mabadiliko ya sheria yanakuja hapa na tumeshaelewana kwamba, kwa kweli ile Sheria ya Work Permit lazima tuipitie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna suala la maagizo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan aliyatoa hapa na ameyarudia tena juzi, nadhani kwenye moja ya hotuba zake kwamba hizi taasisi nyingi ambazo zinafanya kazi katika nchi yetu, hizi katika ku-regulate business lazima zifanyiwe marejeo na alitumia neno ziwe reviewed, maana yake lazima tuzipitie na sisi wenyewe katika Wizara yangu tuna taasisi 15 na moja ya kazi ambayo nimeeleza tunaenda kuifanya katika Wizara yetu ni kupitia hizi taasisi kuona kama kuna muingiliano wa majukumu, ili tuweze kuyaweka vizuri.

Kwa hiyo, tunakwenda kufanya mapitio ya taasisi mbalimbali katika nchi hii ambayo tunadhani yanakwaza biashara, ili tuyaweke vizuri. Hili ni agizo ambalo tunalitekeleza halihitaji sheria yoyote kwa sababu tunalifanya hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumeboresha mifumo ya electronic. Mifumo mingi ya electronic ambayo tunaiona kwa sasa ndani ya BRELA na TBS ni matunda ya utekelezaji wa blueprint. Mifumo mingi ambayo mnaiona kupitia TRA na Wizara ya Fedha na Mipango ni matunda ya utekelezaji wa blueprint. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge inawezekana hatua hazitoshi, lakini sio sahihi sana kusema kwamba hakuna kitu ambacho kimefanyika. Tunafanya mambo mengi, lakini pia, hatupo nyuma ya wakati kwa sababu ndio kwanza action plan imekamilika na utekelezaji unakwenda kuanza katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la mwisho katika hili, mambo mengi ni mindset change, aliongea Mheshimiwa Mbunge Lucy pale. Mengine hayahitaji sheria, hata mimi ninapozungumza na watendaji wangu na wakuu wa taasisi mbalimbali nawaambia pengine tulikosea kutafsiri, hizi bodi zinaitwa regulatory authorities tukatafsiri kwamba ni mamlaka za udhibiti. Sasa udhibiti kiingereza chake ni control, ninawaambia hapana, tunapaswa ku-facilitate sio kudhibiti. Kwa hiyo, mambo mengi ambayo tunayafanya mengine kwa kweli, ni kubadilisha mtazamo tu mtu akae pale akijua kwamba anakwenda kuwezesha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, ndani ya Wizara ya Viwanda na Biashara tumesema tutakwenda kusimamia kitu kinaitwa service charters. Taasisi zetu zote zina mikataba ya huduma kwa wateja na mle ndani tumeainisha huduma hii ichukue muda gani, tunakwenda kusimamia kuhakikisha kwamba huduma zinatolewa mapema iwezekanavyo. Muhimu zaidi nasisitiza kwamba ni kubadilisha mtazamo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ni viwanda vilivyobinafsishwa. Waheshimiwa Wabunge viwanda hivi vipo katika maeneo makubwa matatu, vipo viwanda ambavyo vilitelekezwa; kwa nia njema Serikali ilivibinafsosha tukaingia mikataba na wawekezaji wakavichukua, wakavitelekeza. Yamekuwa mapori, wengine wamebadilisha viwanda hivi kuwa sehemu ya kufugia ng’ombe, wameweka mifugo yamekuwa maghala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mikataba na hawa watu na tulisema wataviendeleza viwanda hivi kwa mujibu wa tulivyokubaliana. Tulipofika hapo Serikali isingekaa kimya na wenyewe kule tulipoenda kuzungumzanao wakasema aa aa, kwa kweli tulikosea chukueni viwanda vyenu; tungefanyaje kwa hiyo, hatujapora wamevirudisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kundi la pili wapo wawekezaji ambao tuliona kwamba hawajaishi vile mkataba ulivyotaka. Tukafanyanao mazungumzo, tukakubaliana wakakiri kwamba tulifanya makosa, wamevunja masharti hapa na hapa, wakakubali kujirekebisha. Hawa tunawarudishia viwanda kwa masharti mapya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wapo ambao wamekubali kwamba kweli tulivunja masharti makubwa na kwa kweli, hatuna uwezo wa kuendelea kufanya hii kazi. Wamevirudisha viwanda 22 hivi ndivyo ambavyo tumevitangaza tunavitafutia wawekezaji wapya na moja ya kipaumbele ambacho tangu niteuliwe nimekipa kikubwa sana ni kusimamia zoezi hili ili viwanda hivi vipate wawekezaji vianze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kundi la mwisho ni viwanda ambavyo kwa kweli tumeshindwa kukubaliana kati ya Serikali na mwekezaji. Yeye anaving’ang’ania anadhani kwamba, yupo sahihi na sisi tunaamini kwamba hayupo sahihi. Sasa nchi hii ni nchi ya utawala wa sheria, katika mazingira hayo tutakwenda kwenye vyombo vya sheria ili tupate haki ama Serikali ama mwekezaji. Hii ndio hatua ambayo tunakwenda nayo katika suala la viwanda ambavyo vimebinafsishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nitolee maelezo mafupi kuhusu suala hili la EPZA na SEZ; Waheshimiwa Wabunge wameongea hapa. Nimeeleza katika hotuba yangu kwamba, moja ya hatua ambayo tunakwenda kufanya, tunakwenda kufanya tathmini ya kina kuhusu mafanikio na changamoto za uwekezaji katika maeneo maalum ya kiuchumi. Hii tathmini itatupa wapi tumefanikiwa, wapi kuna changamoto, nini turekebishe, lakini kwa ujumla wake tathmini ya ndani ambayo tumeifanya uwekezaji katika maeneo haya umekuwa na mafanikio makubwa sana. Mpaka dakika hii tunazungumzia uwekezaji wa dola bilioni
2.5 ni uwekezaji mkubwa, lakini tukifanya tathmini itatupa zaidi tuelekee wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimtoe wasiwasi ndugu yangu Mheshimiwa Getere kuhusu uwekezaji pale Bunda anasema wananchi wake wanakwenda kuwa masikini, hapana. Mwaka huu tumeiagiza EPZA inakwenda kujenga shades kwenye eneo ambalo tumelitenga lile ili viwanda vianze kujengwa pale. Kwa hiyo, Mheshimiwa Getere hapana, watu wako hawatakuwa masikini, tunakwenda kuwekeza pale, tutaweka shades na eneo lile utafiti wa awali unaonesha kwamba ni eneo potential sana, litapata wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kwenye hoja hizi nizungumzie kidogo kuhusu mkakati wa C2C, mkakati wa nguo na mavazi. Waheshimiwa Wabunge wameongea kwa uchungu. Ni kweli karibu nusu ya nchi hii ni wakulima wa pamba, ni zao muhimu. Haikubaliki kama ulivyosema kwamba tuna-export asilimia 30; asilimia 70 ya pamba ambayo tunazalisha hapa. Kumbukeni Waheshimiwa Wabunge mwaka 1992 tulikuwa na viwanda vya nguo 32, lakini mpaka sasa hivi tunazungumza tuna viwanda 12 vya nguo; viwanda nane vya pamba viwanda vingine vilivyobaki vinne vya polister.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na viwanda hivi katikati viliyumba, laki ni kwa kufuatia mkakati wa C2C vingi vimeanza kufanya kazi na juzi nimetoka Morogoro kutembelea baadhi ya viwanda vinafanya kazi vizuri. Muhimu ni kwamba huu mkakati ambao tumeuhuisha, wengi mnafahamu, tumeuhuisha mkakati wetu kwamba sasa unakwenda kutekelezwa kwa miaka mingine kumi, baada ya kuonesha mafanikio makubwa tuna mkakati mwingine mwaka 2021 mpaka mwaka 2031 ili kuhakikisha kwamba viwanda hivi vinasimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini muhimu san ani lile wazo ambalo Mheshimiwa Tabasam amelitoa, ni wazo zuri sana lazima tugawanye. Mchakato wa kutengeneza nguo una hatua karibu sita, lazima tuwe na viwanda vikubwa ambavyo vinapokea kutoka kwenye viwanda vidogo. Tuwe na viwanda ambavyo kazi yao ni ku-feed viwanda vikubwa, unaweza ukawa na viwanda vikubwa vitano tu nchi nzima ambavyo kazi yao ni kumalizia mpaka nguo, lakini viwanda vingine vinachakata kuanzia kwenye kuchambua pamba mpaka kutengeneza uzi na uzi ukaenda kwenye viwanda vikubwa. Tupeni nafasi tutekeleze mkakati huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi mwenyewe kwa kweli mkakati huu ni mzuri sana na ni moja ya kipaumbele katika utekelezaji wangu, ukiona kwenye ile hotuba yangu, ni namba mbili. (Makofi)

Sasa Waheshimiwa Wabunge niwaombe mnipitishie hii bajeti mapema iwezekanavyo, ili mimi kazi hii nianze mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie; kuna Waheshimiwa wamesema hapa hatutembelei viwanda, tunakaa tu ofisini. Waheshimiwa Wabunge mimi nimeapishwa tarehe 9 Aprili, 2021 kama mwezi mmoja umepita, nimeshatembelea tunavyozungumza tayari viwanda vitano. Cha mwisho nimetembelea juzi kiwanda kikubwa sana cha 21st Century pale Morogoro cha nguo, kikubwa kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeshakutana na wadau mara tano, nikiwa hapa Bungeni ndani ya mwezi mmoja tangu niteuliwe. Kwa hiyo, kutembea ni sehemu yetu, kutembelea viwanda, lazima tutembelee viwanda, tukutane na wadau, tuone changamoto zao, tuone mafanikio yao, Mheshimiwa Naibu Waziri kila siku yupo barabarani. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge hili tunalo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la bidhaa la ubora; moja ya taasisi yenye mafanikio makubwa katika nchi hii, na ni vizuri Waheshimiwa tujivunie vitu vyetu, ni TBS. wanafanya kazi kubwa sana kudhibiti ubora wa bidhaa zinazozalishwa ndani ya viwanda vyetu, lakini pia vinavyoingia kutoka nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muhimu sana na mimi nimekutana na wafanyabiashara wengine wanalalamika, ukiwauliza nini, unakuta kwamba ana product yake ambayo ni inferior imekwama test ya kawaida ndani ya TBS, wana maabara tisa za kisasa kabisa. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge tusiwe na shaka tunazo taasisi ambazo zinafanya kazi, wanafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumepokea ushauri wenu kwa maana ya kuboresha na ushauri wa Mheshimiwa pale amezungumzia suala la labeling kuhusu vyakula, wataliangalia kama kuna upungufu tulirekebishe tuimarishe zaidi, lakini kwa ujumla wake nirudie tena, TBS kwa maana ya Shirika letu la Viwango, linafanya kazi nzuri. Ni moja ya mashirika ambayo yanaheshimika sana hapa Barani Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nimtoe wasiwasi tu Mheshimiwa ambaye alizungumzia kuhusu Zanzibar na Tanzania Bara. Tumeshakaa, tumekutana na ndio maana tumekubaliana kwa mfano kwa Zanzibar Bureau of Statistics (ZBS) wamekubaliana na TBS wakipima Zanzibar wakakubaliana kwamba, ni kiwango vizuri hapa Tanzania Bara hakuna haja ya kupima tena. Kwa hiyo, limeshawekwa vizuri, tunafanya mazungumzo ya mara kwa mara kati ya sisi na wenzetu Wazanzibari kuhakikisha kwamba hizi kero ndogo ndogo za muungano ziondoke kwa sababu, sisi ni nchi moja, hilo ndio jambo la msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge tena waridhie ili bajeti yetu ipite tuanze utekelezaji wa kazi. Ninawasalimu tena kwa jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

MWENYEKITI: Toa hoja.

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii. Naomba nichangie kwenye taarifa zetu mbili hasa hii taarifa ya LAAC. Nikiwa sehemu ya Madiwani kule kule ninapotoka, nianze na eneo moja la Mwenendo wa Bajeti na Kiwango cha Utegemezi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, nitambue ukweli kwamba halmashauri nyingi nchini kwa kweli zinajitahidi sana kukusanya mapato kwa kuzingatia makadirio ambayo imejiwekea.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ukiangalia huu mwaka wa fedha ambao CAG ameufanyia audit, 2020/2021, Halmashauri zilipangiwa kukusanya shilingi bilioni 822.38 na zimekusanya bilioni 799.42, sawa na asilimia 94. Kwa hiyo, zinafanya vizuri na kwa nini? Uki- bench mark na Serikali Kuu TRA ilipanga kukusanya trilioni
20.326 ikakusanya trilioni 17.599 sawa na asilimia 86.6. Kwa hivyo, tukilinganisha kiufanisi na kitakwimu halmashauri zetu zilifanya vizuri kuliko Serikali Kuu. Hili ni vizuri tukaliona kwa sababu huwa tunaona tu ule upande wa udhaifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukweli ni kwamba, changamoto za halmashauri zetu sio uwezo wa kukusanya, changamoto kubwa ni ufinyu wa vyanzo vya mapato, hii ndio changamoto kubwa ambayo inatukabili. Ndio maana katika shilingi trilioni zaidi ya 34 kwenye bajeti ambayo tunaijadili, halmashauri zote ukikusanya kwa pamoja hata trilioni moja haziwezi kukusanya, kwa hiyo, ni changamoto kubwa. Tunategemea tu leseni za biashara, service levy, leseni za vileo, vibali vya ujenzi na vibali vya sherehe kwa wale wanaokaa kwenye manispaa na mijini, ukienda vijijini huko wanategemea ushuru wa mazao na kadhalika. Sasa hivi vyanzo ni vidogo ni vifinyu, haviwezi kuifanya halmashauri itekeleze jukumu lake sawasawa kama ambavyo imewekwa katika Katiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chanzo kingine tunafahamu ruzuku, lakini CAG anasema nini kuhusu ruzuku ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri? Mambo matatu; moja kuna halmashauri kama 19 ambazo zenyewe zimepokea ruzuku zaidi ya bajeti yao, kiwango cha shilingi 47.19 na ipo kwenye taarifa ya Kamati yetu. Pili, kuna halmashauri 163 zenyewe zimepokea ruzuku chini ya bajeti yao, yaani imepungua kwa shilingi bilioni 312, lakini tunazo halmashauri 144 ambazo zenyewe hazikupokea kabisa ruzuku ya matumizi ya kawaida. Hii maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ruzuku kimsingi ni hisani, hakuna formula inayotoka Hazina inayotumika kugawa ruzuku, inategemea pengine bidii ya Mkurugenzi mwenyewe, inategemea Meya anaongea vipi na Hazina, ndio maelezo pekee, lakini kwa nini tuwe na variable ya ugawaji wa ruzuku? Hii ni hisani. Je, ni sahihi sisi kama Bunge hili tuendelee kutegemea hisani ya ruzuku? Au tuweke utaratibu mzuri ambao kuna formula inaeleweka na nchi nyingi zimeshaweka, nchi nyingi zimeweka vizuri kabisa kwamba, kila jimbo linapata shilingi ngapi kwa utaratibu upi? Wamefanya hiyo South Africa, wamefanya hivyo Nigeria, wamefanya hivyo juzi wenzetu Kenya kupitia Sera yao ya Devolution. Kwa hiyo nataka niiweke hiyo observation ambayo nadhani ni muhimu sana sisi kama Bunge tukaelewa na tukaizingatia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nipendekeze kutatua hili tatizo kwa sababu tuko kwenye kikao hiki cha hili Bunge hili na hapa hatuishauri Serikali, tunataka kuweka maazimio ili tukasimamie utekelezaji. Naomba nipendekeze mambo matatu na naomba Mwenyekiti wa Kamati kama itampendeza achukue haya mapendekezo, kama ninavyosoma kama ifuatavyo:-

Kwa kuwa Halmashauri zinakabiliwa na uhaba mkubwa wa fedha, mapato kwa ajili ya uendeshaji na miradi ya maendeleo;

Na kwa kuwa ruzuku kutoka Serikali Kuu imekuwa haiendani na bajeti za halmashauri na mara nyingi haipatikani kwa muda muafaka.

Na kwa kuwa vyanzo vingi vya mapato vya kodi vipo kwa Serikali Kuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hii niifafanue, vyanzo vingi vya mapato katika halmashauri vilienda TRA. Tulikuwa tunategemea sana property tax ilienda na juzijuzi tumenyang’anywa ushuru wa mabango na wenyewe hatukusanyi tena na haieleweki sasa hivi anakusanya TANROADS au TRA, lakini halmashauri zimenyang’anywa kukusanya hiyo. Na kwa kuwa kwa hali hii imekuwa ikiathiri uwezo wa halmashauri katika kutekeleza wajibu wake wa kisheria na Kikatiba;

Hivyo basi, Bunge linaazimia kuwa: -

(1) Bunge liweke utaratibu wa kisheria na kikanuni wa kugawana mapato ili kwamba, sehemu ya mapato ya kodi yarudi katika halmashauri. Kama Serikali Kuu tumekubali kwamba, TRA ndio Professional Tax Collectors, lakini TRA hawezi kufanya makusanyo ya property tax bila kushirikisha halmashauri, hivyo tukubaliane kwamba, sehemu ya kodi hiyo irudi halmashauri kwa ajili ya shughuli za maendeleo katika halmashauri ili utaratibu wa kupata hizi fedha uwe ni wa haki, ni wa kisheria kuliko kusubiri hisani ya Hazina.

(2) Kwa kuanzia katika mwaka wa fedha ujao, asilimia 40 ya mapato ya kodi ya majengo na ushuru wa mabango irudi kwenye halmashauri husika; na

(3) Serikali iweke utaratibu na vigezo vya wazi vinavyotumika katika kugawa ruzuku kwa halmashauri ambazo hazina vyanzo vya uhakika vya mapato kwa ajili ya uendeshaji na miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni mapendekezo matatu ambayo nayatoa katika kuboresha jambo hili ili halmashauri zetu ziwe na uhakika wa mapato na kwamba, utolewaji wa ruzuku ufanyike kwa mujibu wa sheria kuliko ilivyo sasa ambapo tunaona kabisa halmashauri hii inapata na nyingine haipati. Hilo ni eneo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili, ambalo limeibuka kwenye Taarifa ya CAG na bahati mbaya sijaliona kwenye Kamati zetu ni suala la mfumo wa udhibiti wa ndani. Usimamizi wa vihatarishi na mfumo wa utawala bora. CAG katika ripoti yake ameibua jambo kubwa sana, ukurasa wa 8-13 anasema, changamoto za mfumo wa uendeshaji wa Serikali za Mitaa amehoji kile ambacho wanaita mwingiliano kati ya Madiwani na mamlaka za utendaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amebainisha kwamba, Madiwani wamekuwa wakishiriki katika shughuli za kiutendaji za mamlaka ikiwemo kwa mfano Wenyeviti na mameya kusaini mikataba na ameona hili jambo sio zuri. Sasa hili tumrejeshe CAG kwenye Ibara ya 145 na Ibara ya 146 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, tumrejeshe CAG kwenye sera ya ugatuaji decentralization by devolution ambayo tuliipitisha mwaka 1996. Tumrejeshe pia kwenye Sheria mbili ambazo zinaongoza Local Government Authority.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mamlaka za Serikali za Mitaa ni Serikali kamili na zipo chini ya Madiwani. Kwa hiyo, ni jambo la muhimu likaeleweka na Waheshimiwa Wabunge hapa sisi ni Madiwani na zile lawama zote ambazo tunazitupa halmashauri ni za kwetu. Sisi ndio wasimamizi, sio tu wasimamizi, sisi ni waendeshaji wa halmashauri tofauti na Serikali hapa, tunaweza tukalaumu Serikali Kuu hapa kwa sababu sisi ni washauri tu, lakini sisi ndio waendeshaji na wasimamizi wa halmashauri kisheria. Sasa kiuhalisia hiyo tutajadili siku nyingine kwamba, kweli sisi tuna nafasi kiasi gani? Hivi kati ya DC na Mkurugenzi, Mkurugenzi akiagizwa akipewa maelekezo na DC anafuata ya nani? Hili tulijadili siku nyingine, lakini kwa sasa tuseme kwamba, Waheshimiwa Wabunge sisi ni Madiwani zile halmashauri zipo chini yetu na kwa jambo hili CAG sio sahihi. Kwa hiyo, azimio hapa liwe ni kwamba:

“Serikali iongeze kasi katika utekelezaji wa sera ya ugatuaji na kuwajengea uwezo wa kutosha Madiwani. Na kwamba, irudishe mamlaka ya Madiwani dhidi ya watumishi.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni jambo la msingi kwa sababu, sasa hivi Madiwani kwa kweli mamlaka dhidi ya watumisi ni madogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kwa sababu ya muda nilisikia kengele hapo. Hili ni la wananchi wa Ubungo kule.

MWENYEKITI: Nimekuongeza dakika mbili Profesa.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ubarikiwe. Ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, tunao Mradi wa DART Dar-es- Salaam, mradi muhimu na unatusaidia sana na tunaupenda, lakini naomba katika suala la kutwaa maeneo ya wananchi wazingatie sheria ya fidia wala wasifanye vinginevyo. Zoezi hili liwe la wazi, liwe shirikishi kama sheria inavyotaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna mgogoro pale Ubungo Kisiwani kaya 91 zinataka kuondolewa. Uthamini ulifanyika katika utaratibu ambao haueleweki, wananchi wamelalamika, Mheshimiwa Rais ametoa shilingi bilioni 7.8 kwa ajili ya fidia, lakini watu wa DART wameshindwa kusimamia utaratibu mzuri wa kuweka utaratibu pale kwa ajili ya fidia. Mheshimiwa Waziri tumelizungumza hili naomba alifuatilie ili wananchi wale watendewe haki, wapishe mradi, fidia ilipwe kwa mujibu wa sheria. Hili ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dakika moja iliyobaki nichukue nafasi hii kuzipongeza sana Kamati zetu mbili kwa kazi kubwa, ripoti zao ni nzuri sana. Tupongeze vilevile halmashauri zetu kwa sababu, kwa mara ya kwanza wamepata hati inayoridhisha asilimia 96. Ukiangalia kwa miaka mitano hiyo record haijawahi kuvunjwa, kwa hiyo, ni jambo jema, halmashauri zetu zinafanya kazi katika mazingira magumu, tuwatie moyo, tuwasimamie wafanye vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale wanapofanya vizuri tuweze kuwatia moyo, kwa hiyo, hili ni jambo zuri ambalo nadhani kwamba, ni muhimu likazungumzwa. Hii ni sawa na waliopata kwenye upande wa Serikali Kuu, lakini la mwisho, bahati mbaya mapendekezo mengi hayatekelezwi yale ya CAG na CAG analalamika kwamba, mapendekezo mengi yamekaa bila kutekelezwa. Azimio moja tupendekeze hapa ni kwamba, pengine kuanzia mwaka ujao wa fedha pale ambapo Mamlaka ya Serikali za Mitaa au Mamlaka ya Serikali Kuu haijatekeleza angalau asilimia 50 ya mapendekezo ya CAG, watu hawa waitwe kwenye Kamati yetu ya Haki na Maadili wajieleze na hatua stahiki zichukuliwe ili tuokoe fedha za wananchi wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya malalamiko mengi ambayo tunayatoa hapa CAG ametoa mapendekezo namna ya kuyashughulikia, watu hawatekelezi. Bahati mbaya hawajachukuliwa hatua yoyote criminal kwa sababu, CAG report sio criminal document ni jambo nadhani kwamba, sisi kama Bunge tutake watu hawa waitwe. Kama mtu anaweza akaitwa kwenye Kamati kwa kosa dogo, kama amefuja fedha za wananchi aitwe kwenye Kamati yetu ya Haki na Maadili ili ajieleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na mimi kwa kunipa nafasi hii kuchangia maeneo haya mawili katika maazimio yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze mchango wangu kwenye hiba. Hiba ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, hiba ni urithi au waingereza wanasema legacy. Hili naamini wasomi wataandika kwa muda mrefu ujao kwaajili ya kuweka kumbukumbu sawasawa; mchango ambao Mheshimiwa Rais wetu wa Tano alitoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa duniani maisha yetu ni mafupi, na kifo cha Dkt. Magufuli kinatukumbusha kwamba hapa duniani Maisha yetu ni mafupi sana. Muhimu sana kwa kweli ni kwamba, sio kwamba tutakufa au la, kufa tutakufa, lakini tukifa tunapoondoka tutakumbukwa kwa lipi? Mwenzetu kwa kweli ameondoka akiwa ameacha alama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa duniani tunaambiwa kuwa kuna mambo mawili, kuna kutoa na kupokea. Wengi wetu huwa tunapokea, lakini tunapata baraka kwa kutoa, mwenzetu ametoa, ametoa maisha yake, ametoa kupitia mchango mkubwa wa kazi zake ambazo tutaendelea kuziishi kwa muda mrefu bila kuorodhesha mambo mengi ambayo ameyafanya ambayo watu wengi wameyasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, na uteuzi wa leo wa Makamu wa Rais ni jibu na ujumbe kwamba kazi inaendelea. Hilo ndilo jibu ambalo tunapewa kwamba, ni stability and continuity. Kwamba kitabu kinaendelea kuandikwa tunaendelea kwenye ukurasa mwingine. Tunashukuru sana kwa uteuzi ambao Mheshimiwa Rais ameufanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kifo hiki kinatukumbusha miaka 20 iliyopita. Tarehe 4 Julai, 2001 nchi yetu ilikumbwa pia na msiba wa Makamu wa Rais Dkt. Omari Ali Juma. Mheshimiwa Mkapa alipomteua Dkt. Ali Mohamed Shein alitoa sababu kwa nini amemteua. Alitoa sababu sita ambazo kwa kweli ukizirejea, ndizo unazoziona leo kwa viongozi wetu wawili wakuu; kwa maana ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, lakini hata uteuzi wa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa ruhusa yako naomba nizirejee hizo sifa sita ambazo zilimuongoza Mheshimiwa Mkapa kumteua Mheshimiwa Ali Mohamed Shein. Yeye alisema kwamba, Watanzania wanatarajia sifa zifuatazo kutoka kwa viongozi wao; na ameandika pia kwenye kitabu chake kwamba ndivyo kigezo cha viongozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sifa ya kwanza ni utu na uadilifu. Yamesemwa hapa kuhusu utu na uadilifu wa Mama Samia lakini pia wa Mheshimiwa Dkt. Mpango. Upendo na heshima kwa watu wote. Kupenda kazi na kutumikia wananchi badala ya kupenda kutumikiwa na kukuzwa. Watu wengi wenye vyeo tuna shida moja. Ukiwa na cheo kuna mawili, unataka watu wakikuona wakuone nini? Wakimuona Kitila wamuone Kitila kwanza Waziri baadaye, ama Waziri kwanza Kitila baadaye? Watu wengi wanataka waonwe kwanza kwa vyeo vyao, halafu baadaye wao. Hapa Mheshimiwa Mkapa anasema, kiongozi mzuri ni yule ambaye anataka kwanza kabla ya cheo chake watu wamuone yeye, na hii ni sifa ya msingi ambayo viongozi wetu wawili wanayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naiweka vile vile namba nne, kuweka mbele maslahi ya taifa na Watanzania badala ya maslahi binafsi, viongozi wetu tunawafahamu vizuri. Unyenyekevu, limezungumzwa sana hili, viongozi wetu wawili Mheshimiwa Rais tangu aanze kazi hii; na watu wanaomfahamu kabla tuliopata nafasi na bahati ya kufanya naye kazi kabla tunafahamu unyenyekevu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho ni kuzingatia misingi ya Taifa; na aliitaja misingi tisa; utu, haki, usawa, fursa sawa, amani, umoja, upendo, mshikamano na hii ya mwisho aliandika kwa herufi kubwa MUUNGANO. Kiongozi yeyote katika nchi hii lazima tukimuona, tukimuangalia, tukimsikia tuwe na hakika kwamba Muungano wetu upo salama. Hakuna shaka kwamba kwa viongozi wetu wawili hawa Muungano wetu upo salama sana. Na hilo ni jambo la msingi mno. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ni ukuu wa Katiba yetu. Watu wamelizungumza hili na limezungumzwa sana lakini sidhani ni kwa uzito ambao tunapaswa kuuona. Marekani wameshafiwa na Marais nane, wakiwa madarakani tangu mwaka 1841 na juzi 1993; na muda wote walikuwa na changamoto ya namna ya kumuapisha Makamu wa Rais, wamehangaika wameweza kufanikiwa kufanya mabadiliko 25 mwaka 1967. Sisi walioandika Katiba Mungu awabariki. Katiba yetu ina ukuu wa pekee, tumepita katika kipindi kigumu wala tusijue kwasababu Katiba yetu na misingi ipo salama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamtakia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan na Makamu wa Rais na viongozi wote neema na baraka na mafanikio tele katika uongozi wao. Mungu awabariki sana. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nami nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri sana aliyoitoa jana hasa kwa matumizi yake ya picha na video ambayo yalionesha wazi kwamba kazi kubwa inaendelea katika sehemu mbalimbali hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, bahari mbaya Mheshimiwa Waziri Mkuu jana alisahau au aliamua kuacha kwa makusudi tu, moja ya mafanikio muhimu sana alipokuwa anazungumzia eneo la utamaduni, sanaa na michezo. Ukweli wenyewe ni kwamba, kwa hakika mwaka huu tena Yanga itachukua ubingwa wa Ligi Kuu ya NBC. Kwa hiyo, alitaja pale mengi lakini hili akaliacha, sasa nimeona nilitaje. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mwaka huu na mwezi huu wa Aprili, nchi yetu inaadhimisha miaka 100 ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kama angekuwa hai, mwezi huu angefikisha miaka 100. Ni fursa nzuri kwa nchi yetu kuendelea kutafakari mchango wa Mwalimu, lakini pia ni fursa nzuri kuendelea kutafakari historia ya nchi yetu; miaka 60 ya Uhuru wa Tanganyika na miaka 58 ya Muungano wetu wa Tanganyika na Zanzibar. Siku ya Jumatatu tarehe 29 Julai, mwaka 1985, Mwalimu alitoa hotuba yake ya mwisho katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania akiwa Rais. Katika hotuba ile alitumia nafasi ile kuipitisha nchi katika mafanikio yaliyopatikana katika uongozi wake na katika changamoto ambazo zilijitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, moja ya jambo zuri sana katika hotuba ile, ni ukweli kwamba Mwalimu alikuwa muwazi na mkweli kwa makosa ambayo aliyafanya katika uongozi wake. Alitaja mengi, lakini muhimu yanajitokeza wazi. Moja, alikiri na alitumia neno la Kiingereza, alisema: “it was a major error kufuta Mamlaka za Serikali za Mitaa.” Kosa la pili ambalo aliliita: “the other most serious mistake,” ilikuwa ni kufuta Vyama vya Ushirika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kosa la kwanza tulilisahisha yeye mwenyewe akiwemo mwaka 1982 kwa Bunge hili kutunga Sheria ya Kurejesha Mamlaka ya Serikali za Mitaa na tukaingiza kwenye Katiba ibara 145 na 146. Pia tumefanya marekebisho makubwa tangu wakati huo hasa mwaka 1996 - 1998 pale ambapo tuliamua kuanza kutekeleza Policy ya D By D (Decentralization by Devolution) maarufu kama Sera ya Ugatuaji wa Madaraka Mikoani.

Mheshimiwa Spika, sera hii ina mambo makubwa mawili. Kwanza ni kuhamisha majukumu ya kusimamia matumizi ya fedha za maendeleo na watumishi kutoka Serikali Kuu kwenda Serikali za Mitaa. La pili, tuliona kabisa kwamba huduma za jamii ili ziweze kuwa endelevu; zingekuwa tu endelevu kama wananchi wangeshiriki kikamilifu katika kubuni kwa maana ya kuibua miradi, kushiriki kwenye utekelezaji wake na kuisimamia pale ambapo imeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, kwa maoni yangu, tuna mambo matatu ya kusahihisha katika eneo hili la Local Government. Kwanza ni kuhusu mahusiano kati ya Serikali Kuu na Serikali ya Mitaa. Ukisoma ile document, mahusiano yanayotarajiwa kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa ni mahusiano ya kiushauri na kiuwezeshaji; kwamba Serikali Kuu itaishauri na kuiwezesha Local Government.

Mheshimiwa Spika, zimetoka tathmini za wataalam, tena report imetoka juzi tu ya wataalam wetu hapa nchini, wanatueleza; na uhalisia Wabunge wanafahamu. Uhusiano uliopo kati ya Local Government zetu na Serikali Kuu hasa kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI ni wa kimaelekezo; kwamba kazi kubwa ya Serikali Kuu ni kuelekeza mamlaka zile na mamlaka kutekeleza. Kwa hiyo, siyo ushauri. Hivyo, ile dhana ya kwanza ya kuipa mamlaka Serikali za Mitaa inapotea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ni muhimu, ni kiwango kidogo cha ushirikishwaji wa wananchi katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Tulisema wananchi washiriki kwenye kuibua na kutekeleza miradi ya maendeleo. Kwa sasa kwa kweli ukifuatilia kwa karibu, na tathmini zinaonesha hivyo, wananchi wengi wamekuwa wapokeaji na washangiliaji wa mafanikio ya miradi ya maendeleo. Ushiriki unazidi kupungua.

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ni lile ambalo pia kwenye hotuba ya Mwalimu amelizungumza. Kwa wakati wake aliona kwamba changamoto na sifa zote zilikuwa zinaelekezwa kwake. Ni kwamba changamoto zote ni kwake na zikitokea sifa za mafanikio zinaelekezwa kwake. Jambo hili halikumpendeza na akalikemea. Naomba ninukuu maneno yake aliyoyasema. Alisema kwa Kiingereza: “our President is important, but he is not Tanzania. The Vice President and the President of Zanzibar are important, but they are not Tanzania. We; all of our people organized together, are Tanzania.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nasisitiza kwamba ni muhimu kwa wananchi kushiriki kikamilifu katika ujenzi wa miradi ya maendeleo na mafanikio yanayopatikana. Pia pale ambapo mafanikio yanapatikana ni muhimu sana wananchi waonekane kwamba ni sehemu ya mafanikio. Ni muhimu sana Halmashauri zetu zionekane kwamba ni sehemu ya mafanikio.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani mradi wa maendeleo utekelezwe Kakonko halafu sifa zote ziende Serikali Kuu, sifa zote ziende kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, sifa zote ziende kwa Waziri Mkuu, sifa zote ziende kwa Mheshimiwa Rais, siyo sahihi. Lazima utukufu wa mafanikio pia ugawanywe ili ile sense of ownership iwepo miongoni mwa wananchi. Kwa sababu wanapoona kuwa miradi tumetekeleza, tumesifiwa sisi, mafanikio ni yetu, ile sense of ownership inakuwepo. Vilevile changamoto zikitokea, haiwezekani changamoto zote zimetokea, tumwelekeze mtu mmoja au watu wawili. Lazima tuwe na sense of ownership ya changamoto na mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu la kurekebisha ni lile ambalo limejitokeza. Tumesema tunatekeleza Sera ya Ugatuaji, lakini ukweli ni kwamba hii inaitwa devolution. Wataalam wa Local Government sasa wanasema kinachoendelea siyo devolution, isipokuwa ni deconcentration, kwa maana umemega madaraka kidogo yakashuka kule chini. Nami naita ile ni ugutuaji, siyo ugatuaji ni ugutuaji. Turudi kwenye sera yetu ya msingi ya ugatuaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ambalo nataka kuchangia kwa sababu kengele ya kwanza imegonga, ni eneo hili ambalo Mheshimiwa Waziri Mkuu amelieleza kwenye hotuba yake ukurasa wa 78 mpaka 83. Ni hoja kuhusu upandaji wa bei za bidhaa na hatua ambazo Serikali inazichukua; nami naunga mkono zile hatua ambazo amezieleza pale ikiwemo kudhibiti wafanyabiashara wasipandishe bei holela. Pia ameeleza vizuri sababu za mfumuko wa bei na bei ya mafuta kupanda.

Mheshimiwa Spika, maelezo ni mazuri, lakini maelezo peke yake hayatoshi. Muhimu sana kwa Serikali ni kwamba Serikali inachukua hatua gani kuwapunguzia wananchi makali ya maisha kutokana na kupanda kwa bei? Hili ni jambo la msingi. Sote tunajua bei zimepanda katika hali ambayo siyo ya kawaida. Chukua mfano, kati ya Aprili mwaka 2020/2021 bei ya mafuta ilipanda kwa wastani wa shilingi 36, lakini Aprili, 2021/2022 hii ya juzi, imepanda kwa shilingi 738. Siyo kiwango cha kawaida cha upandaji wa bei ya mafuta. Sote tunatambua kwamba siyo kwa sababu yetu au Serikali, lakini hoja ya msingi kwa Serikali ni kwamba, inachukua hatua gani kuwapunguzia wananchi makali? Waingereza wana msemo unaosema, desperate times calls for desperate measures. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maoni yangu ni kwamba tuko katika kipindi ambacho siyo cha kawaida na Serikali lazima ichukue hatua ambazo siyo za kawaida. Ushauri wangu hapo ni kwamba Waziri wa Fedha na Mipango na Kamati yetu ya bajeti, haraka iwezekanavyo wakae waangalie katika bajeti yetu ni wapi tunaweza kuchukua hatua za kusaidia?

Mheshimiwa Spika, mapendekezo yangu ni kwamba katika zile levy, shilingi 792 ambazo zinakusanywa moja kwa moja kama Levy kwenye mafuta, Kamati ya Bajeti inaweza ikashauri tukachukua shilingi 300/= mpaka shilingi 400/=, tukaondoa kwa muda mfupi kwa miezi mitatu au minne tukitarajia kwamba mwezi Julai mpaka Agosti, kwa jinsi wataalam wanavyosema, hali itarudi kama kawaida. Tukifanya hivyo, tutakuwa tumempunguzia mwananchi ukali wa maisha. Hizo fedha ambazo zinapungua kwenye miradi ya maendeleo, sasa hivi Serikari yetu bahati nzuri inakopesheka, ikope ili miradi ya maendeleo isisimame. Hayo ndiyo mapendekezo yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, narudia tena, desperate times calls for desperate measures. Hatupo katika hali ya kawaida, lazima Bunge lako lichukue hatua ambazo siyo za kawaida. Inapofika wakati wananchi wanaumia, msemaji wao mkubwa katika nchi ni Bunge. (Makofi)

MheshimiwaSpika, Bunge hili haliwezi kukaa kimya; haliwezi kuridhika tu na maelezo ya Serikali kwamba maelezo bei zimepanda kwa sababu moja, mbili, tatu; haitoshi. Muhimu sana tunachukua hatua gani kupunguza makali ya maisha kwa wananchi? Hili ndilo jambo la msingi, na Serikali hii ambayo inaongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa jinsi alivyoonesha upendo mkubwa kwa wananchi wake, naamini tukimshauri atachukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, uongozi mpya siku zote ni fursa na sisi tuna fursa hapa ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan na fursa imejitokeza. Nakumbuka maono yake yameshatolewa katika maeneo makubwa mawili, kwanza katika hotuba ambayo ilitolewa hapa Bungeni mwaka 2021, ya pili ni kwenye Makala ambayo aliiandika tarehe 01, Julai, 2022. Makala ambayo alikuwa anaakisi miaka 30 ya mfumo wa demokrasia ya vyama vingi nchini ambapo aliibuka, nataka kunukuu hapa, alieleza kuwa: - "Ndiyo sababu kwenye uongozi wangu ninaamini katika kile kinachojulikana kama 4R – ikiwa ni ufupisho wa maneno manne ya Lugha ya Kiingereza; Reconciliation (Maridhiano), Resilience (Ustahamilivu), Reforms (Mabadiliko) na Rebuilding (Kujenga Upya)" mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni matumaini yangu kwamba wenzetu Serikalini, Mawaziri, watakapoleta bajeti zao hapa tutaona jinsi ambavyo wametafsiri ndoto hii ya Mheshimiwa Rais kupitia mipango na bajeti ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa leo nataka nizungumzie eneo moja katika hizo 4R, R ya tatu ambayo ni reforms (mabadiliko). Na Mheshimiwa Rais alisema kuwa nimedhamiria kwamba kwenye kuenzi miaka yetu ya demokrasia ya vyama vingi, Serikali yangu itajitahidi kufanya mabadiliko katika mifumo ya kisiasa, kiuchumi na katika sheria. Lengo ni kwamba Tanzania yetu iende na wakati” mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katiba yetu Ibara ya 6 inatambua Serikali tatu, aina tatu za Serikali katika nchi hii; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Serikali za Mitaa. Hizi ndizo aina tatu za Serikali. Na zote zina Rais wake; Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yupo, Rais wa SMZ yupo na Rais wa Serikali za Mitaa bahati nzuri ni huyohuyo wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeweka sheria mbalimbali kwenye kutafsiri maono haya ya Katiba; Sheria ya Serikali za Mitaa tunafahamu Sura Na. 287 na 288 kwa maana ya wilaya na miji. Tumeweka sera ya ugatuaji, na sera hii tumekuwa tukiitekeleza tangu mwaka 1998. Ililenga kuhamisha na kupeleka madaraka katika maeneo makubwa mawili, kutoka Serikali kuu kwenda ngazi ya halmashauri za wilaya, miji, manispaa na majiji. Pili, kutoka ngazi ya halmashauri kwenda kwenye ngazi za msingi za kata, mitaa, vijiji na vitongoji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma hii inazungumzia vertical decentralization, haizungumzii horizontal decentralization. Lakini sisi kwenye tafsiri yetu, tulichofanya tuka-decentralize kutoka Wizara ya Maji, kutoka Wizara ya Elimu kwenda Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo bado ni central. Kwa kutumia falsafa ya Mheshimiwa Rais ya reform lazima tuliangalie upya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, decentralization ilikwamia sehemu haijafika mwisho, na ndiyo maana wakurugenzi kila kukicha safari zao kutoka Ubungo, kutoka Songea kuja Dodoma. Wako wapi; kwenye kikao Dodoma, kwa sababu Mamlaka za Serikali za Mitaa hazifanyi kazi yake sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sheria tumeweka vyombo vitatu vya kutekeleza hili. Cha kwanza tumesema Baraza la Madiwani ndicho chombo cha juu cha maamuzi katika halmashaui. Sasa Waheshimiwa Madiwani wenzangu mliopo hapa niwaulize; hivi kweli Baraza la Madiwani katika halmashauri zetu ndicho chombo cha juu cha maamuzi? Ndivyo ilivyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema ya pili Kamati ya Maendeleo ya Kata (Ward Development Committee) ndicho chombo cha maamuzi katika ngazi ya kata ambapo Mwenyekiti wake ni Diwani. Na mwisho tumesema Mwenyekiti wa Kijiji/Mtaa ndiye kiongozi na Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, sheria na sera zipo vizuri sana, tunahitaji reform kuhakikisha kwamba sera hizi zinafanya kazi sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nipendekeze maeneo matatu ya reform; kwanza tuna changamoto ya kwanza kati ya viongozi wachaguliwa, wateule na waajiriwa. Tukienda kwenye uchaguzi tunachagua viongozi watatu; tunamchagua Rais, Mbunge na Diwani. Inapokuja kwenye utekelezaji wa majukumu, Rais ni msimamizi wa shughuli za Serikali katika Serikali Kuu na kwa vitendo anaonekana hivyo, lakini Diwani ambaye ni msimamizi katika kata yuko wapi? Hili ni eneo la reform ambalo lazima tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili; Madiwani kisheria tumewapa jukumu la usimamizi wa programu za maendeleo katika ngazi ya kata. Kisheria ndio wakuu katika shughuli zetu za maendeleo. Tukawaongezea pia jukumu la kusimamia ukusanyaji wa mapato katika kata zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Madiwani ni part time workers. Umewahi kuona wapi duniani mtu umekabidhi jukumu la usimamizi halafu ni part time? Hili ni eneo ambalo lazima tuliangalie, linahitaji reform. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwenyekiti wa Kijiji ambaye ndio kiongozi na mkuu wa Serikali, huyu naye ni parttime, lakini kwenye kata tukaenda tukarundika. Nilikuwa naangalia muundo wa kata moja pale Dar es Salaam, ofisi ya kata moja ina watumishi 16, watawala saba, afya wawili, elimu wawili, maendeleo ya jamii mmoja, afisa ustawi wa jamii mmoja, kilimo mmoja, mifugo mmoja, uvuvi mmoja. Dar es Salaam afisa uvuvi kwenye kata anafanya nini? Dar es Salaam afisa mifugo kwenye kata anafanya nini? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunahitaji reform, hawa watu wapunguzwe ili mshahara unaotokana na hawa tumpe Diwani awe fulltime worker. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kama tupo serious na local government authority, Madiwani ni muhimu wawe wafanyakazi wa kudumu wawe salary, wapewe mishahara, kwa sababu hawa, sisi angalau kwenye Bunge ni wakutoa ushauri. Diwani sio wa kutoa ushauri ni msimamizi inakuaje msimamizi asiwe mfanyakazi wa kudumu? Tunahitaji eneo hili lifanyiwe reform...

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimwia Naibu Spika Taarifa.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Vivyo hivyo mkuu wa Serikali ya Kijiji na mtaa. Mkuu wa Serikali ya Mtaa unamfanyaje kuwa part-time?

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Huyu naye lazima tufanye rationalization ili kwamba huyu naye awe ni sehemu ya utumishi katika eneo lake.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kitila kuna taarifa.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika,naomba nimpe taarifa mazungumzaji Profesa Mkumbo; najua ni mwanafunzi mzuri sana wa decentralization na nimewahi ku-share naye kwamba decentralization…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa twende kwenye taarifa.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa nimpe taarifa tu kwamba kwa mfumo wa ugatuaji wa Serikali za mitaa nchini hauiondoi Serikali za mitaa kwenye unitary government. Pamoja na kuwa kuna hayo mamlaka ambayo tumewapa hawa madiwani lakini mfumo hautoi madiwani kuwa na workforce ya kumwezesha kutekeleza majukumu ambayo anajaribu kuyazungumza. Ndiyo maana kwenye ngazi hiyo wameweka wataalam wa kada mbalimbali kama ilivyo kwenye Wizara, Waziri ni mmoja, Naibu ni mmoja lakini kuna katibu mkuu na watendaji tofauti wa kumsaidia ku discharge majukumu ya Serikali kwenye ngazi ile hautegemei majukumu yale afanye mwanasiasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.

NAIBU SPIKA: Ahsante, Mheshimiwa Mkumbo.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, Siipokei hiyo taarifa kwa sababu inakinzana na hoja yangu, kwa hiyo sipokei hata kidogo. Lakini hoja ya msingi ameipata, mimi ni mwanafunzi wake mzuri wa local government, sasa amenifundisha mwenyewe halafu ananipinga, haiwezekani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya msingi ni kwamba wale watu ambao wanafanya kazi za kila siku za kusimamia maendeleo yetu ili tuone impact kwenye government reform ni muhimu sana wakapewa majukumu yao na yaendane na hadhi yao, wapewe wafanye kazi zao za msingi ikiwemo utumishi wa kudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho na mimi nichukue nafasi hii kumpongeza sana kwa mkitadha huu Mheshimiwa Rais kwa kuja na haya mambo manne (4R) na kwakweli Waheshimiwa Wabunge sisi tunajukumu la kutafsiri hizi 4R za Mheshimiwa Rais hapa ndani na katika utendaji wa Serikali. Mwisho nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa jinsi anavyomsaidia Mheshimiwa Rais kwenye kusimamia shughuli za maendeleo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante, kengele ya pili.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. PROFESA KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, na kwa kweli nianze mchango wangu kwa kukupongeza, unaendesha kikao vizuri sana. Upo vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue nafasi hii kwa kweli kupongeza sana hatua ya Serikali na Mheshimiwa Rais kutoa kibali cha ajira 21,000. Jambo hili siyo la kupongeza tu kwa maana ya utaratibu wa kawaida. Katika kipindi ambacho dunia nzima ina changamoto ya kiuchumi, katika kipindi ambacho kuna nchi tunavyozungumza leo zimeshindwa kulipa mishahara ya watumishi, katika nchi ambazo zimeshindwa kulipa mishahara ya Waheshimiwa Wabunge, lakini sisi siyo kwamba tunalipa tu mishahara, tunaajiri watumishi wapya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili haliwezi kupita bila kuzungumziwa vizuri. Ni jambo kubwa, na ni jambo jema. Tunatambua kwamba idadi ya ajira hizi siyo kwamba zinakidhi, lakini lazima kila hatua tuone kwamba ni hatua na sisi kama Wabunge lazima tupongeze na kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tukishashukuru tunajenga hoja ya kuongezewa zaidi kwa hiyo hilo ni jambo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili katika hoja hiyohiyo, viongozi hufanya mambo manne; hujenga, huboresha, hufanya mambo mapya na hurekebisha pale ambapo walipoishia wenzao hapakukaa vizuri. Namimi nataka nichukue nafasi hii, hata hili la kuajiri ni hatua kubwa ya Mheshimiwa Rais ya kurekebisha kwa sababu miaka mitano, sita, saba nchi hii ilikuwa haiajari watumishi. Hawa waliyotoka vyuo vikuu wanafahamu, miaka ya tisini, miaka kumi Serikali iliacha kuajiri watumishi hasa katika vyuo vikuu kwa kitendo hiki ni hatua nzuri ya kurekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika muktadha huohuo nataka niombe Serikali warekebishe mambo mengine mengi lakini hasa matatu katika utumishi wa umma, na nataka kuzungumzia utumishi katika vyuo vikuu; kwa sababu pia kwenye Jimbo la Ubungo pale kuna Chuo Kikuu cha Kwanza Tanzania (Chuo Kikuu cha Dar es salaam) ambapo nimewahi kupata bahati ya kukitumikia; kwa sababu kufanya kazi chuo kikuu kama Profesa ni bahati kubwa na mshukuru Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa chuo kikuu kwa walimu ni uhuru wa kitaaluma (academic freedom). Yaani mwalimu chuo kikuu lazima anapokaa pale awe na uhuru wa kufundisha na kufanya utafiti na kusambaza maarifa bila woga wa kufikili kwamba hataingiliwa, ataonewa, atashughulikiwa, atabaguliwa au atanyanyaswa; huu ni msingi ambao unaongoza vyuo Vikuu Vyote Duniani. Ni kwa sababu vyuo vikuu duniani vinakuwa na sheria zake; na sisi tungekuwa na sheria ya vyuo vikuu, kila chuo kingekuwa na sheria yake. Hata hivyo mwaka 2005 Bunge likatunga Sheria linaitwa Universities Act, Sheria Na. 07 ya Mwaka 2005, lengo ni kulinda uhuru wa kitaaluma katika vyuo vikuu. Na vyuo vikuu vimeanzisha vyombo vyao vya kujiendesha na kujitawala. Kwa hiyo kazi kubwa ya Serikali imekuwa ni kutoa sera na muelekeo na kutoa rasilimali lakini uendeshaji wa vyuo vikuu unakuwa ndani ya vyuo vikuu vyenyewe. Kwa hiyo kuna vyombo viwili vikubwa; Kuna Baraza la Chuo Kikuu na kuna Senate, Senate ni kama Bunge hili. Hili ni jambo la msingi sana ambalo lazima tulielewe, na hivyo hivyo duniani. Sasa hizi nyenzo zimewekwa ili vyuo vikuu vijiendeshe na vilinde uhuru wa kitaaluma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo jambo moja la msingi sana ambalo lazima tulirekebishe ni kuepusha urasimu wa kawaida kuuingiza vyuo vikuu, bureaucracy ya kiserikali. Kwa mfano vyuo vikuu duniani na hapa Tanzania siku zote huwa vinaajiri watumishi wake; na ndiyo maana kwenye sheria yetu ambayo nimeisoma function namba 05 ya mabaraza ya vyuo vikuu is to appoint officers of the institutions. Maana yake waajiri wa vyuo vikuu ni mabaraza ya vyuo vikuu, na ajira za chuo kikuu ni za chuo husika. Ndivyo ilivyo duniani, ndiyo maana inaitwa university, yaani universal from the word universal). Kwamba misingi ya vyuo vikuu ambayo inafanana duniani kote. Sasa nataka niulize, na mtusaidie kulirekebisha jambo hili. Katika miaka ya hivi karibuni, nadhani kuanzia Mwaka 2015, 2016, tumeamua ajira za vyuo vyuo vikuu zinaendeshwa na Serikali kupitia Sekretarieti ya Ajira. Hili jambo ni peculiar kwa Tanzania, halipo vyuo vikuu vyovyote duniani. Yaani huwezi; na naona mmeanza kuhamisha walimu kutoka chuo kimoja kwenda chuo kingine. Mwalimu wa Chuo Kikuu cha Oxford akitaka kwenda Cambridge ana- apply, anaomba aajiriwe na Cambridge; lakini huwezi kukuta Serikali ina muamisha huyo mtu kutoka Chuo Kikuu cha Cambridge kwenda Oxford, hiyo Duniani haipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili jambo lazima mliangalie, muachie vyombo ambavyo tumeunda kisheria kufanya ajira. Hata hizi ajira za walimu ambazo tunalizungumza hapa, tunaona kama jambo la kawaida, kwamba wanaajiri Ofisi ya Rais – TAMISEMI lakini sheria haisemi hivyo. Sheria ya Ajira za Walimu ipo katika Tanzania Teacher’s Service Commission, na ipo very clear. Moja ya majukumu ya Commission TSC jukumu namba 03 is to appoint, promote and discipline teachers. Kwa hiyo Waziri ana jukumu la kurebisha hapa; na Mheshimiwa Rais moja ya ajenda yake nikufanya maboresho na marekebisho tumsaidie kurekebisha. Moja ya marekebisho ni kwamba Utumishi waache vyombo vya kisheria vifanye kazi zake. (Makofi)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Taarifa Mwenyekiti.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Getere taarifa.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa maelezo ya mzungumzaji, kwamba kuna Sheria ya Kuajiri Walimu kupitia Tume ya Walimu tunaomba ajira inayoendelea sasa hivi ifutwe tufate sheria iliyopo sasa hivi. (Makofi/Vicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kitila Mkumbo, unapokea Taarifa?

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Nimeipokea ni muhimu Serikali ikafanya marekebisho na maboresho. Kama sheria hizi ambazo tunatunga mnaona hazifanyi kazi leteni tufanye mabadiliko, ni jambo la msingi kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambalo linaendana na hilo, na nataka niweke msisitizo kabisa kabisa; mnaanza kuhamisha walimu kutoka vyuo vikuu kwenda chuo kikuu kingine; hili nimeisha lisema siyo sahihi. Ajira za walimu ni za chuo husika. Kitila Mkumbo akita kwenda chuo kikuu cha UDOM ana apply. Sasa nyie mmehamisha walimu kutoka Chuo Kikuu cha Dar es salaam; kwa mfano a rarely professor environmental economics mmemtoa pale mkaenda kumtupa Chuo Kikuu cha Mwalimu Julius K. Nyerere cha Kilimo na Teknolojia ambacho hakina wanafunzi, yupo pale hana wanafunzi. This is a professor ambayo alikuwa anafanya kazi vizuri sana pale chou kikuu. Mmemuamisha mwalimu ametoka PHD resource assessment ana uchungu wa kufanya kazi amekaa siku mbili tatu ana hamishwa kwenye Chuo cha Maji, kufanya nini? Kwa hiyo kaka yangu Ndugu yangu Mheshimiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kitila Mkumbo, nakuongeza dakika nne ili uweze kumalizia hoja yako. (Makofi)

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ubarikiwe sana, uko vizuri. Hilo nadhani limeeleweka; Mheshimiwa George Simbachawene tunakuheshimu, umefanya kazi nzuri naomba hili jambo ulifanyie kazi ulirekebishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni ajira za mikataba kwa maprofesa wa vyuo vikuu. Tulikuwa na utaratibu mzuri sana, Profesa akisha ku–retire chuo kikuu, vyuo vikuu vinamfanyia tathimini. Akiwa bado ana nguvu na anafanya kazi zake kitaaluma vizuri anapewa mkataba wa miaka miwili miwili mpaka pale tutakapoona kwamba afya yake ya mwili na kiakili imechoka. Jambo hili tukaliondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ipo hivi; profesa si kama wana michezo, ambaye kadri umri unavyokwenda anazidi kuchoka. Uprofesa ni kama wine. Wine inavyokaa muda mrefu ndivyo inavyozidi kunoga, profesa unavyozidi kukaa muda mrefu anazidi kubobea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na maprofesa wengi, wanafahamu Profesa Ndalichako, maprofesa wengi wanapata uprofesa late 50’s na wameongezewa hadi 60’s. Sisi wengine tuliopata tukiwa na miaka 40 tulibahatisha tu, lakini Maprofesa wengi wanapata Uprofesa miaka 50 na kuendelea. Sasa amemaliza tu profesa ndiyo anaanza kubobea mnamuondoa. Kwa hiyo tunaomba utaratibu wa zamani ambapo Profesa akishakustaafu anapewa mkataba uendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uliopo madhara yake ni nini? Vyuo vikuu vya umma kwa sasa vinaanza kubaki na junior staff. Kwa sababu Maprofesa wote ambao wana– retire Chuo Kikuu cha Dar es salaam wanakwenda kwenye private universities; tunamsaidia nani? Kwa hiyo naomba hili pia Mheshimiwa Waziri aliangalie na alirekebishe lirudishwe kwenye utaratibu ambao ulikuwepo. Kwa sababu tunasema if it is not broken don’t fixed it, kwa sababu ni kitu kizuri kilisaidia nchi yetu, kilisaidia vyuo vikuu vyetu. Utaratibu huu kwa nini uliondolewa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni kuwaombea. Wametufata maprofesa wa siku nyingi ambao waliajiriwa kabla ya mwaka 1978 kabla ya PPF kuanzishwa; hawa watu hawakuwa kwenye mfumo wa pension, waliwekwa katika mfumo wa bima, wanalipwa kitu kinaitwa SSSS (Serious Staff Superannuation Scheme). Hawa maprofesa wameondoka chou kikuu anapata milioni 10, milioni 20. Baadhi yao wameniambia hata ukitaja majina yetu ni sawa tu. Sasa wamebaki maprofesa 180, hawana pension, wapo tu. Jambo hili limieshawasilishwa mara nyingi, Serikali imelipokea, hivyo tunaomba Mheshimiwa George Simbachawene kupitia kiti chako jambo hili ulimalizie ili tutunze heshima ya watu ambao wametumikia katika nchi hili miaka 30, miaka 40 katika utumishi wa vyuo vikuu, ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kusema hayo nimalizie tena kukushukuru na kukupongeza kwa mchango wako naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukurukwa nafasi hii na mimi. Kwanza nitumie nafasi hii kwa kweli kuishukuru na kuipongeza Serikali na Rais wetu kwa kufanikisha kuwaondoa Watanzania kule Sudan katika uwanja wa vita; jambo hili limetujengea heshima. Hawakuondoa Watanzani tu lakini pia wameondoa raia wenzetu katika nchi nyingine za Kiafrika; na dunia yote ijue kwamba hisia ambayo iliasisiwa na mwalimu Nyerere ikaongoza ukombozi wa Bara la Afrika bado ni ile ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili na mimi nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Madini na timu yake kwa kazi nzuri ya kusimamia sera na sheria za madini. Nilikuwa naangalia ule mpango wa maendeleo, nadhani ni moja ya Wizara chache ambazo zinaelekea kukamilisha lengo la mpango wa maendeleo ambao tumesema sekta hii ichangie asilimia kumi; kwa jinsi ambavyo tunakwenda tunaweza kufikia hapo. Kwa hiyo tunashukuru na kuwapongeza kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niweke mchango wangu katika eneo moja tu. Ni suala la nafasi ya sekta ya madini kwenye kupambana na umaskini kwenye nchi hii. Hakuna shaka kitakwimu tunakwenda vizuri lakini ukweli ni kwamba sekta hii bado haijatusaidia kwenye kutuondoa kwenye umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nchi zote ambazo zimeendelea ni kwa sababu ya mambo mawili tu ama zina rasilimali watu au na asilimali asili na sisi tunayo rasilimali watu lakini tuna hii moja rasilimali asili muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano, mwezi uliopita, huu Februari kulikuwa na mkutano mkubwa sana pale Cape town South Africa, Engaba Mining Conference. Kwenye mkutano ule kwa mara ya kwanza Marekani ilipeleka ujumbe mkubwa sana; na ilimtuma mwakilishi wao maarufu Amos Horsen ambaye ni mwakilishi maalum kabisa wa Rais Joe Biden katika sekta ya madini, na hawakuficha. Malengo yao ni mawili, moja Marekani inataka kuona kwamba inatumia sekta ya madini kutatua changamoto za mabadiliko ya tabianchi hapa duniani lakini pili imeweka wazi kwamba imeshangazwa na imeshtushwa na ukweli kwamba kwa sasa biashara kwenye sekta ya madini kwa kiasi kikubwa inatawaliwa na China, kwa hiyo wanataka kuwa-take over.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake ni kwamba kuna vita kubwa ya madini inakuja. Haya mataifa mawili yakishaamua kupambana kuna vita inakuja uko mbele. Wametaja madini kwa mfano Lithium, graphite, Nickel, Cobalt, wameyataja haya ndio madini wanayalenga. Jumla wameainisha aina hamsini za madini; maana yake ni nini, ni kwamba kuna haja ya kuangalia upya model yetu ya uendeshaji wa madini hapa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshapitia hatua tatu, kwanza tulianza na wakoloni, walipokuja wakoloni hapa Waingereza ule mradi wa Mwadui, wanafahamu watu wa madini, walikuwa wanamiliki De Beers ailimia 50, Serikali ya Uingereza asilimia 50. Sisi tulipokuja kwenye Azimio la Arusha tukatangaza kwamba madini yote katika nchi hii yatakuwa chini ya Serikali, ndipo tukaunda STAMICO. Haikufanya vizuri sana na sababu zinajulikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miaka ya 1990 tukahama tukaenda kwenye ubinafsishaji, na tukasema kazi ya Serikali ni kukusanya kodi na kuweka mazingira ya kuvutia wawekezaji basi, uchimbaji na kadhalika waende sekta binafsi. Hii ikatuletea matatizo, ndiyo ikatubakishia mashimo, hatujafaidika sana miaka 20 ya sera hiyo. Naiyo maana mwaka 2015 na 2017 tumekuja na Sheria hizo mbili, tumezitekeleza, tumebadilisha na tumefaidika kwa kiasi. Hata hivyo, kwakweli ambacho kimebadilika kikubwa tumebadilisha sana numbers lakini bado suala la umiliki liko mikononi mwa wawekezaji na wawekezaji wa nje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mapendekezo yangu ni kwamba ile sera ambayo tulikuwa nayo mwanzoni, hapa tulipofika Serikali na sisi kama Bunge tukubaliane kuchagua baadhi ya madini ambayo piga ua asilimia mia moja yatakuwa chini ya Serikali. Bahati nzuri Mheshimiwa Waziri mwenyewe kwenye hotuba yake ameshaainisha madini haya yapo vanadium, Nickel, Graphite, yametajwa pale, vizuri kabisa; na hii ambayo ameongea Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria hapo ya mambo ya Liganga na Mchuchuma, tuwekeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia uwekezaji, ukiangalia katika miaka, wenzetu wa Tume ya Madini wameanisha madini mengi pale lakini nimechagua saba. Thamani ya uwekezaji wa madini haya kwa miaka kumi mpaka ishirini ijayo ni bilioni 4.385 sawa na tirioni kumi. Mauzo yatakayotokana na uwekezaji huu ni dola za Kimarekani bilioni 63, hii ni GDP ya Tanzania kwa sasa almost, sawa na trilioni 145. Sisi tutapata nini? Tutapata dola bilioni 17 sawa na trilioni 39 asilimia 27, sijui kama unanielewa hapo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani uwekezaji wote huo tutaambulia asilimia 27 ambayo ni chini hata ya corporate tax; na hapa tumeshachukua royalty, inspection fee, corporate tax, kodi zote, tutaishia kupata tirioni 39; na haya ni madini ambayo ni muhimu sana. Zipo nickel na lithium humo. Kwa hiyo ninachotaka kupendekeza hapa ni kwamba, tubadilishe model ili baadhi ya madini yaende STAMICO, STAMICO imarishwe, ipewe mtaji, ipewe watu sahihi ili iwe hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na itakuwa siyo sisi peke yetu, wanafanya hivyo Botwana. Botswana yale madini yote ya dhahabu yapo chini ya Debswana Company Limited ambayo ni ya Serikali kwa asilimia mia moja. Botswana madini ya dhahabu hayachimbwi na private sector. Ukienda India wanayo NMBC, South Africa ambayo tunaiona hapo wakati wa Makaburu waliijenga tunayoiona ile kwa sababu ya dhahabu, na walikuwa wanamiliki Makaburu wenyewe. Kwa hiyo hii model ambayo tunayo tuchague baadhi ya madini tuwe na model tatu. Uwekezaji upo, ipo ya hamsini kwa hamsini lakini ya tatu asilimia mia moja yawe ya kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mwisho ni suala la umakini kwa wataalam wetu katika ushauri tunaoutoa kwa Serikali. Hapa tunapoongea nchi yetu ipo kwenye disputes mbalimbali za kimataifa ambazo zinatokana na uwekezaji. Nilikuwa napitia website ya dispute and judgement navigator, tuna kesi takriban saba, tatu za madini. Kampuni ya Montero, Nachingwea, Wisher tumeshitakiwa kule na watu wamepeleka madini; lakini ukiangalia sababu ni kwamba watalam wetu walitushauri wakaishauri Serikali hii, wakasema kwamba baada ya kubadilisha Mining Act ya 2017, wakabadilisha zile regulation 2018, wakashauri kwamba leseni ambazo zilikuwepo zifutwe, zile provisional license, wakasema hakutakuwa na shida, lakini shida ipo. Sasa wasomi wetu walete ushauri wa kisomi sio ushauri wa kishujaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa sekondari kulikuwa na methali inasema kwa mwoga huenda kicheko na kwa shujaa huenda kilio. Wale wanafunzi tuliokuwa tukisoma nao wanajifanya hawataki kusoma, hawasomi kwa bidii, wanakwenda disco wanajifanya mashujaa; akitoka disco anakwenda kwenye mtihani. Wale ambao walikuwa wanasoma wanaambiwa wanoko wanafanya revision kwa umakini wanafaulu, wale wanaopata division four, division zero wanalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wa kishujaa ndio huo. Kwamba unamwambia kiongozi hakuna shida usiwe na wasiwasi, humwambii ukweli, tunaingia kwenye kesi hizi na sasa hivi Serikali inalipa fedha nyingi. Wasomi wetu watupe ushauri wa kisomi. Ushauri wa kisomi ukweli ni kwamba huwa ni mchungu; unamwambia kiongozi ushauri ni mchungu, lakini ushauri wa kishujaa unampa kiongozi anachokitaka ili afurahi akupendelee sasa ushauri huo ni ushauri ambao hautusaidii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya madini imejaa wataalam wazuri wanajulikana nchi hii; hebu watueleze ukweli ni nini, tusiingize nchi yetu kwenye matatizo makubwa. Si sahihi kabisa kutoa ushauri wa kishujaa ambao siku hizi ushauri wa kishujaa unaitwa ushauri wa kichawa, huo si mzuri na hautusaidii kama nchi. Kwa hiyo ni jambo ambalo niliona niliweke mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti,lakini mwisho, ameongea Mwenyekiti wa Sheria pale; hili la Liganga na Mchuchuma sipendi kuliongelea kwa sababu na mimi nilishapitia huko, wanafahamu Mheshimiwa Kakunda na Mheshimiwa Mwijage, ni heshima kubwa. Ule mradi investment cost yake ni bilioni tatu, kwa nini Serikali kupitia STAMICO, kutokana na umuhimu wa mradi huu; kwa nini tusiachane na mambo ya uwekezaji na tutafute fedha, tukope tuwekeze kwenye mradi huu? Kama Serikali imekubali kukopa mradi wa SGR, imekubali kukopa kwenye mradi wa bwawa ambao returns yake ni long term, mradi huu ukishakamilika tunaanza kupata fedha sasa, hii ni muhimu kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa mradi huu utatupa investment ni three billion lakini kwa mwaka tutakuwa tunapata more than 1.4 billion dollars. Kwa hiyo maana yake ndani ya miaka kumi tumepata Dola za Marekani bilioni 14; sasa tatizo ni nini? Kwa hiyo naomba Mheshimiwa wa Madini na Waziri wa Viwanda ile failure ambayo sisi tuliowahi kuwa mawaziri kwenye sekta hii tumepitia naomba iwaepuke kabisa. Shaurini mamlaka, tuachane na uwekezaji kwenye sekta, hii Serikali ikope fedha tuwekeze wenyewe ili Watanzania waweze kufaidika na mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuniahidi kunipatia Chuo cha VETA kwenye Jimbo la Ubungo kwa sababu huwezi kuwa na kiwanda cha pili kwa ukubwa cha kutengeneza nguo, kinaajiri zaidi ya watu 4,000, unayo pale EPZA kubwa kuliko zote Tanzania ipo pale na Naibu Waziri anayeshughulikia kazi anafahamu alishafika pale. Kwa hiyo kuna vijana wengi, hivyo, nashukuru sana kwa kuniahidi kwamba tutashirikiana tupate Chuo cha VETA kwenye Jimbo la Ubungo hususan Kata ya Makuburi ambapo ina high concentration ya viwanda hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo nataka niongeze sauti yangu ni kwenye suala ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelichangia kwa hisia kubwa, suala la lugha ya kufundishia. Kwanza nianze kwa kuungana mkono kabisa na jinsi ambavyo sera imependekeza, nadhani iko sahihi kabisa kwamba lugha zetu mbili zitatumika kufundishia Kiswahili kwenye ngazi ya chini na Kiingereza kwenye ngazi inayofuata.

Mheshimiwa Spika, suala la mjadala hili huwa lina sehemu mbili tu. Unaweza ukajadili kwa kuzingatia uzalendo wa lugha na utamaduni, hiyo ni sawa pia, hawa wanaita cultural romanticism, lakini unaweza kujadili pia kwa kuangalia taaluma. Nadhani sisi hapa kwa maana ya sera tunaangalia taaluma na kuangalia tunazingatia kupanua wigo kwa vijana wetu lakini pia hali halisi. Hali halisi ni nini? Moja ni makosa, kudhani kwamba Kiingereza ni lugha ya wakoloni, ilishaisha siku nyingi.

Mheshimiwa Spika, Waingereza wapo milioni 67 tu tunavyozungumza, lakini duniani hapa kuna watu bilioni moja wanaotumia Kiingereza kama lugha ya kwanza. Kwa hiyo Kiingereza kuwa lugha ya wakoloni iliisha siku nyingi ndio maana kuna Kiingereza cha West Afrika, Kiingereza cha South Africa, Kiingereza cha Kenya, Kiingereza cha Scandinavian kuonyesha kwamba Kiingereza kwenye lugha ya ukoloni kilishaondoka lakini sikiliza takwimu zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, asilimia 53 ya tovuti kwa maana ya website zote duniani zinatumia lugha ya Kiingereza. Lugha ambazo zinafuata ni chini ya asilimia 10. Kwa mfano, Kichina hiki ambacho watu wanakizungumza sana hapa asilimia mbili tu, Kifaransa asilimia nne, Kirusi asilimia sita, Kijerumani asilimia sita, Kihispaniola asilimia tano, Kireno asilimia tatu. Asilimia 53 iko kwa lugha ya Kiingereza, hiyo nakwambia kwamba lugha ya Kiingereza imeendelea kuwa lugha ya taaluma na biashara duniani. Ndio maana Lufthansa ambalo ni shirika kubwa la ndege lipo Ujerumani na Ujerumani ni Taifa ambalo ni very conservative kwenye lugha, lakini waliamua kubadilisha policy yao mwaka 2010 kufanya kwamba lugha ya Lufthansa ni Kiingereza kwa sababu ndio lugha ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hilo tuondoke kwenye uzalendo wa lugha, hii sio lugha tena ya wakoloni. La pili, katika nchi kumi zenye mfumo bora wa elimu Afrika, nazizungumzia Seychelles, Mauritius, Afrika ya Kusini, Botswana, Kenya, Cape Verde na Namibia. Nchi saba zinatumia Kiingereza kama lugha ya kufundishia na tatu zinatumia Kiarabu hizi ni Algeria, Tunisia na Misri. Pengine niwape mfano wa karibu hapa Afrika nchi ambazo zinasemekana kama ni bora kwa elimu ni Seychelles na Mauritius na zinafanana na sisi, kwa sababu wale wana lugha Yao, Seychelles na Mauritius lugha yao ni Krioli ndio lugha ya Taifa, lakini lugha yao ya kufundishia ni Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ukiingia mtaani, mtaani hutosikia Kiingereza ni Krioli lakini kwa Seychelles wanaanza na Krioli mpaka primary kama sisi, wakifika sekondari all the way ni Kiingereza. Mauritius wenyewe tangu awali wanaanza na Kiingereza all the way lakini ndio nchi ambazo tunazungumza zipo bora katika suala la elimu. Nchi 47 duniani zinatumia Kiingereza kama lugha ya kufundishia, kwa hiyo usije ukadhani ni hapa tu na nchi 143 duniani Kiingereza ni somo la lazima.

Mheshimiwa Spika, tazama kwa hapa Tanzania, nikupe takwimu hii na unisikilize kwa makini sana hii. Ukichambua takwimu za matokeo ya darasa la saba ambayo tunatumia Kiswahili miaka mitatu iliyopita, ukiangalia shule pale, kwa mfano Dar es Salaam, ukichukua shule 50 za juu ambazo zimefanya vizuri, shule ya kwanza mpaka ya 50 zote zinatumia Kiingereza kama lugha ya kufundishia ikiwemo shule ya Msingi Olympio ya Serikali ambayo ni moja ya shule za Serikali ambazo zinatumia Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hiyo maana yake nini? Hatuwezi kulaumu Kiingereza kama ndio chanzo ya wanafunzi kufeli, sio kweli, kwa sababu shule za msingi zinatumia Kiswahili, lakini tafuta shule 50 bora utakuta ni zile ambazo wanatumia Kiingereza.

MBUNGE FULANI: Aliongea bila kutumia kipaza sauti.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Hilo sitaki kusema.

Mheshimiwa Spika, tunapoandaa mitaala tunaangalia factors nyingi. Moja ya msingi ambayo lazima uzingatie mtaala wowote lazima uzingatie matakwa ya wazazi, wazazi wanataka nini na tuna takwimu mbili hapa. Kabla shule za binafsi hazijapamba moto Tanzania, Watanzania middle class wengi wakiwepo Wabunge hapa walikuwa wanawapeleka watoto wao Uganda na Kenya, walikua hawafuati elimu, walikua wanafuata Kiingereza. Baada ya shule kuanzishwa hapa wamerudi.

Mheshimiwa Spika, takwimu ya pili tulishafanya utafiti kati ya mwaka 2015 mpaka 2017, tuliwauliza wazazi, mngetaka watoto wako wafundishwe kwa lugha gani, asilimia 63 yaani wazazi sita mpaka saba kati ya kumi walisema walitaka watoto wao wafundishe kwa Kiingereza kuanzia awali mpaka chuo kikuu na utafiti wa mwaka jana, wa karibuni unaonyesha kwamba ni asilimia 70. Kwa hivyo ukiwa Waziri wa Elimu unapotengeneza mtaala huwezi kutengeneza mtaala ambao upo mbali na matakwa ya wazazi, wazazi ni sehemu muhimu sana kwenye suala hili.

Mheshimiwa Spika, hapa nazungumza nini? Ninachosema hapa hakuna shaka kwamba lugha ni nyezo muhimu sana kwenye suala la elimu na ni muhimu watoto na Walimu watumie lugha ambayo wanaijua, lakini lugha huzaliwi nayo, lugha unaipata kwenye mazingira hili ni jambo la msingi ambalo tunatakiwa tulizingatie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo na hatusemi hakuna tatizo la lugha Tanzania, la Kiswahili na Kiingereza, lipo, ni kubwa, lakini jambo la msingi hutatui tatizo kwa kulikimbia, unalitatua kwa kulikabili. Hapa nataka nipendekeze kwamba, maadam sera imeshaelekeza hivyo, hatua mbili lazima zichukuliwe. Hatua ya kwanza lazima tukubali kwamba tuna changamoto kubwa sana ya Walimu kwenye somo la Kiingereza, kwa maana ya idadi na hata ubora wao. Sasa nchi zingine walifanyaje na mimi nilipitia pitia, walipoamua kwenda mfumo ambao tunataka kwenda nao, walikiri tatizo, lakini jambo la pili waliamua kufungulia milango.

Mheshimiwa Spika, nataka kushauri kwamba Serikali itumie nafasi ya uwepo wa protocol ya hii ambayo tunazungumzia ya free movement of labor tumeshafungua East Africa. Sisi tunauza Kiswahili, sisi ndio wababe wa Kiswahili katika Bara la Afrika lakini wapo wenzetu ambao wametutangulia kwenye Kiingereza, tufungulie mipaka, miaka mitano mpaka 10 waje Walimu hapa kutoka ndani ya Nchi za Afrika, waje Walimu hapa wa Kiingereza wale tunawapelekea Kiswahili tunakarabisha Walimu wa Kiingereza. Ndani ya miaka mitano mpaka kumi tatizo hili litakuwa limekwisha.

Mheshimiwa Spika, nadhani hili ni jambo la msingi, kwa hiyo tuombe Wizara ya Elimu, lakini pia Ofisi ya Waziri Mkuu pale kwenye Ofisi ya Kamishna wa Labor kwa sababu wako very rigid, pale kupata vibali vya kazi ni kazi ngumu sana. Kwenye suala la elimu lazima walipitie upya, tu-relax ili tupate Walimu wengi wa somo la Kiingereza kutoka Nchi zingine. Itakuwa ni hatari sana Mheshimiwa Waziri tukabadilisha sera, tukabaki na sera ambayo tunayo ya kutumia Kiingereza halafu tusiwe na wafundishaji wazuri wa Kiingereza, itakuwa ni hatari kwa nchi, tutakuwa tumetwanga maji kwenye kinu. Kwa hiyo suala moja muhimu tuwekeze sana kwenye suala hili la Walimu wa somo hili la Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, nataka kusisitiza kwamba hakuna shaka, tunakipenda Kiswahili chetu. Tunachosema ni kwamba watoto wa Kitanzania hapa walipofika lazima wawe Kiingereza kizuri, Kiswahili kizuri na itafika mahali hata kitabu kitakuwa kwa lugha ya Kiswahili kwa lugha ya Kiingereza. Akisoma Archimedes Principle haielewi anafungua Kiswahili. Hata mtihani ukija hakuna tatizo lolote, anapewa mtihani upo kwa Kiingereza upo kwa Kiswahili. Akiona anaweza akajibu kwa Kiswahili vizuri anafanya kwa Kiswahili wala hatuna sababu, muhimu ni kwamba maarifa yapatikane kwa lugha mbili hizi, Kiswahili na Kiingereza na lugha isiwe kikwazo kwenye kupata elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa jinsi ambavyo walirejea kwenye ripoti yetu kwenye suala hili. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge Kuhusu Pendekezo la Kuridhiwa Mkataba Baina ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Dubai kwa Lengo la Kuanzisha Ushirikiano wa Kiuchumi na Kijamii katika Uendelezaji wa Maeneo ya Bandari Nchini
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia tena wa kwanza, muda ukiniruhusu nitakuwa na maeneo matano.

Mheshimiwa Spika, kwanza, ni suala la msingi wa kisera; Chama cha Mapinduzi kilibadili mwelekeo wa kisera za kiuchumi na kisiasa miaka ya 1990 na mabadiliko mojawapo yaliyokuwa kwenye sera za kiuchumi ni kwamba tuliachana na sera za Serikali kuhodhi nyenzo za uchumi kama ilivyokuwa kabla.

Mheshimiwa Spika, miaka 20 ya CCM ilifanya tathimini kuhusu utekelezaji wa sera zake na mwaka huo ikatoa tafsiri ya ubinafsishaji na inasomeka hivi; “Ubinafsishaji hauna maana ya Serikali kukabidhi mali ya umma kwa watu au taasisi binafsi. Ubinafsishsji maana yake ni mambo matatu yafuatayo:-

(i) Kuanza ama kuuza baadhi ya hisa za kampuni za umma kwa wawekezaji binafsi; ama

(ii) Kuingia ubia na makampuni binafsi au watu binafsi wa ndani au nje ya nchi;

(iii) Kukodisha kampuni ya umma kwa taasisi au watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, hii ndio misingi ya sera ya ubinafsishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkutano Mkuu wa CCM wa Nne uliweka mazingatio mawili katika Sera ya Ubinafsishaji; kwanza, ni Serikali kuchagua taasisi au mtu binafsi kwa uangalifu ili awe mtu au tassisi yenye uwezo wa fedha na teknolojia, ujuzi wa biashara wa soko linalohusika na manufaa kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, Mkutano Mkuu ulielekeza kwamba mashirika na rasilimali muhimu ambao ni msingi na nyeti kwa maendeleo ya Taifa yanaendelewa kumilikiwa na dola. Mkutano Mkuu ukataja mashirika hayo na rasilimali hizo kwamba ni pamoja na Bandari, Reli, Posta na Simu na Nishati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kwa sababu hii mpaka leo TANESCO inamilikiwa na Serikali asilimia 100, ni kwa sababu hii Reli inamilikwa na Serikali, ni kwa sababu hii Bandari, Posta na Simu kwa maana ya TTCL inamilikiwa na Serikali. Kwa maelezo hayo azimio lililopo mezani lipo ndani ya sera za msingi za kiuchumi za CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, azimio hili lililopo mezani halihusu Bandari kuuzwa, azimio lililopo mezani linahusu uendelezaji na uboreshaji wa utendaji wa bandari. Chama cha Mapinduzi kisingeruhusu Serikali yake kuingiza azimio hapo la kuuza bandari kwa sababu ni mali ya Serikali, lakini Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM kamwe asingeruhusu kuingiza humu azimio ambalo linauza bandari kwa sababu ni kinyume na sera yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia Wabunge hawa walioko hapa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wala wasingepokea azimio la namna hiyo. Kwa hiyo tuwatoe wasiwasi Watanzania tunachojadili hapa kipo ndani ya misingi ya kisera za kiuchumi za CCM. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni hofu ambayo imejitokeza; kwa unyeti wa bandari mara baada ya kusikia taarifa hizi za kubinafsisha bandari, wananchi wengi waliingia hofu na kusema kweli sisi kama Wabunge lazima tuzipokee, kuzielewa na kuzishughulikia hofu na hisia za watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sisi tunafanya mambo yetu hapa na kuzingatia mambo mengine ambayo ni matakwa ya wananchi wetu. Kwa hiyo, hizo hofu ni lazima tuzishughulikie na ninaamini baada ya Bunge hili tutakuwa tumefanya kazi kubwa ya kutoa hofu za wananchi wetu kuhusu jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli kimsingi tangu tuanze ubinafsishsji hakuna jambo ambalo limewahi kupokelewa bila hofu. Mtakumbuka wakati tunabinafsisha NBC kulikuwa na hofu kubwa na mjadala ulikuwa ni mkubwa sana. Mtakumbuka mpaka TBL na TCC hiki kiwanda cha Sigara ilikuwa ni mjadala mkubwa. Mimi nakumbuka nilikuwa chuo kikuu mwaka 2005/2006 tuliamua ku-beggar eneo kwa ajili ya kujenga Mlimani City, tuliambiwa Chuo Kikuu kimeuzwa, lakini tulisimama imara, Rais Kikwete akatusimamia. Sidhani kama leo kuna Mtanzania atalalamika kuhusu Mlimani City. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hofu ya pili inayoeleweka lazima tukubali kwamba hatuna historia nzuri sana kwenye ubinafsishaji. Kutokana na historia ya baadhi ya mambo wananchi waliingia hofu kwa sababu katika baadhi maeneo tulipigwa kwa kweli lazima tukiri, na kwa sababu hiyo hofu zinaeleweka na hofu hii Mheshimiwa Mkapa aliwahi kuieleza wakati wa NBC. Baada ya kelele kubwa sana za NBC Rais Mkapa alitulia akauliza tatizo ni nini? Ndipo akarekebisha wakati wa NMB. Ndio maana akauliza nifanyeje, akashauriwa kwamba NMB Serikali iwe na ubia, lakini vilevile ili ipate mtaji, watumishi wako wote wa Serikali na wengine wapitishie mtaji NMB. Ndio maana unaona leo NMB ni taasisi imara na inafanya kazi vizuri sana. (Makofi)

Kwa hiyo, katika mchakato wa ubinafsishaji Serikali imekuwa ikirekebisha pale panapohitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, sitaki kulizungumzia sana kwa sababu Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri wamekwishaeleza kwamba azimio linahusu nini. Azimio hili kama alivyosema Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri tunazungumzia kuanzisha mahusiano ya kiuchumi na kijamii kati ya nchi mbili Serikali yetu na Serikali ya Dubai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo tukisharidhia Serikali inakwenda kufanya kazi yake ya kawaida ya kuingia kwenye mikataba. Kwa hiyo, hapa tulipo waheshimwa wananchi hatuna mkataba wa TPA na DP World, wala hiyo sio kazi ya Bunge hili hiyo ni kazi ya Serikali. Kwa hiyo, hilo jambo lieleweke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukisoma Mkataba huu kama alivyosoma Mheshimiwa Mwenyekiti na Mheshimiwa Waziri appendix I inazungumzia maeneo tutakayoingia kwenye miradi ni Bandari ya Dar es Salaam, akifanya vizuri Serikali inaweza kumwalika ndivyo mkataba unavyosema aende kwenye maeneo mengine. So, it is not automatic tunazungumzia Bandari ya Dar es salaam na baadhi ya maeneo, Berth Zero, Berth Four, Berth One to Four, Berth Five to Seven, kwa hiyo, ipo wazi jambo hili lieleweke.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne, Waheshimiwa Wabunge, sisi kama Wabunge tuna jukumu pale ambapo kunakuwa na upungufu kwa kuzingatia hisia za watu na hofu zao na mapendekezo yao kurekebisha pale ambapo inahitajika kurekebisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka kupendekeza kwa kuzingatia Ibara ya 22 kwa sababu watu pia wanasema Mkataba huu hauna namna ya kurekebisha. Mkataba unarekebishika kwa Ibara ya 22 imeweka wazi kwamba inawezekana kurekebeshika, kwa sababu kengele imelia nitaachia hapo, lakini nataka kupendekeza maeneo ya kurekebisha ikafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Spika, moja ni suala la timeframe; hili limezungumzwa sana na wananchi kwamba mkataba hauna timeframe na wataalamu wetu wametoa maelezo kwamba mikataba ya namna hii kimataifa ni kawaida kutokuwa na timeframe. Hata hivyo, waende wakaangalie sisi ni Bunge la Taifa wala sisi sio Bunge la Kimataifa, kama hizo ndizo hisia a wananchi na ndio matakwa ya wananchi, angalieni uwezekano wa kurekebisha hata mkisema not exceeding 25 years that is fine ili kutoa hiyo hofu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni Ibara ya 23(4) kile kipengele kingeweza kuondoka kile ambacho kinaaeleza kwamba mkataba hauvunjiki. Kimsingi Mkataba unavunjika mle mle ndani. Kwa hiyo, waangalie lugha iliyotumika ili kuwaaminisha wananchi wa Tanzania kwamba inawezkana kuvunja Mkataba.

Mheshimiwa Spika, jambo la tano na mwisho, ni mambo ya kuzingatia kwenye mikataba ijayo kwa wataalamu wetu, yapo mengi lakini la kwanza, kwenye ile bandari yetu pale kwenye appendix I, kimsingi ni maeneo ambayo tumekwishafanya uwekezaji. Kwa hiyo, tunatarajia mkataba ambao mtakaoingia uta–focus zaidi kwenye eneo la uendeshaji kuliko uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, pili, kwa maoni yangu ni maeneo ya mifumo ya TEHAMA; hili ni eneo sensitive linahusu usalama wa nchi, tuombe sana watu watu wa TCRA na e-Government wawepo, asiachiwe mwekezaji peke yake. Lazima watu wetu wahusike kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, kila nchi kuna nchi zimebahatika kuwa na waasisi, nyingine hazina. Sisi ni moja ya nchi ambazo tuna waasisi kama ilivyo Marekani wana George Washngton - Rais wao wa kwanza aliwaachia misingi. Msingi mkubwa ambao Marekani wanaulinda kwa wivu mkubwa ni liberty kwa sababu ndio walioachiwa kwa maana ya uhuru wa watu wao.

Mheshimiwa Spika, sisi tuna waasisi nchi hii, Julius Kambarage Nyerere na Sheikh Abeid Karume ndio waasisi wa Taifa hili, na walituachia misingi kama ambavyo ilivyo kwa Marekani tunapaswa tusiiguse. Msingi mama wa Taifa hili mwalimu alisema; “silaha na sifa yetu kubwa ni umoja.” (Makofi)

Kwa hiyo, nchi yetu ni mfumo wa demokrasia ya vyama vingi, bila shaka tutatofautiana kimtazamo kuhusu sera na mikakati, lakini kamwe tofauti zetu zisiende kugusa misingi mama ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi Kitila Mkumbo natoka Kijiji cha Mgela, Kata ya Mtoa, Tarafa ya Ishedede Wilaya ya Iramba - Singida lakini mimi ni Mbunge wa Jimbo la Ubungo - Dar es Salaam, hilo limewezekana kwa sababu ya umoja wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna nchi ambazo Wabunge wao ni Wabunge wa makabila sio Tanzania, tunataka na tunatamani huko tuendako watoto wangu, watoto wa wajukuu zangu mimi atoke Iramba akagombee Ubunge Pemba, atoke Pemba akagombee Ubunge Bukoba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuwaombe na tuwasihi wanasiasa na sisi viongozi tuepuke kauli na ambazo zinagusa misingi mama, tutofautiane kisera, hiyo inatosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kwa dakika moja tu naomba nitoe wito kwa wataalamu wetu. Wataalamu wetu mmesikia hofu, hisia na matamanio ya Watanzania. Watanzania hawapingi ubinafsishaji wa bandari wanataka mikataba iwe mizuri, kwa hiyo wataalamu wetu hilo lizingatiwe. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo nilikuwa nakusikiliza mchango wako. Samahani hapa mwishoni hapa badala ya hili neno ubinafsishaji linaweza tena kutuma ujumbe mwingine. Nadhani kuna tofauti ya uwekezaji na ubinafsishaji. Hitimisha hoja yako kwa sekunde thelathini.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo wataalamu wetu mzingatie hilo ili uwekezaji uwe mzuri.

Mheshimiwa Spika, mwisho tuliombe Bunge lako la kuanza nalo katika mikataba itakayoingiwa tuombe ije hapa kwa mujibu wa sheria tuliyonayo kwa sababu ni nyeti na ni muhimu mikataba hii ije tuipitie kama ambavyo sheria inasema itakuwa ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, na mimi nishukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja tatu. Nitakuwa na mambo manne, la kwanza ni muktadha, muktadha ni kwamba humu ndani Bungeni tuna Waheshimiwa Wabunge sisi wote lakini pia kuna Serikali na kila mtu apewe nafasi ya kufanya kazi yake. Kazi ya msingi ya Mheshimiwa Mbunge ni kuhoji Serikali. Kazi ya sisi tuliopo huku ni jukumu letu la msingi kujibu hoja za Wabunge. (Makofi)

Kwa hiyo, tunaposimama kujibu hoja za Wabunge isionekane kwamba tunatetea majambazi, haiwezekani, Serikali ya CCM ilishafunga Mawaziri. Kwa hiyo, suala la kupeleka majambazi na wezi mahakamani halijaanza leo lipo. Wapo Mawaziri, wapo Makatibu Wakuu walishafikishwa mahakamani, muhimu ni kwamba sheria lazima zizingatiwe. Kwa hiyo, nataka kuweka vizuri hili kwamba tunapofanya shughuli yetu ya msingi ya kujibu baadhi ya hoja za Waheshimiwa Wabunge isionekane kwamba tunafanya makosa kama ambavyo Waheshimiwa Wabunge mnahoji kama jukumu lenu na sisi tuna haki ya kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Kwa hiyo, tupewe nafasi hiyo. (Makofi)

Katika Taarifa ya CAG mambo ya msingi tunakubaliana na kwa kweli hamna Waziri hapa anayebishia Ripoti ya CAG, lakini kuna hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wamezisema mimi kama Waziri wa Serikali ninawajibika kuzijibu. Kwa mfano, mtu anasema naomba ninukuu; “na leo nasisitiza kuwa tumepigwa zaidi trilioni 280.”

Mimi kama Waziri wa Mipango ninayefahamu kwamba pato la Taifa lote nchi hii ni shilingi trilioni 141, nitaacha vipi kujibu hoja hii? Yaani kutoka Kagera mpaka Pemba, ukikusanya fedha zote za Watanzania ni shilingi trilioni 141. Mtu anasema zimepigwa trilioni 280 how? Logic inakataa. Kwenye argument kuna kitu kinaitwa fallacy, kwamba premise and conclusion lazima zioane pale zikigongana ina kuwa inconsistency inakuwa ni mkanganyiko huo ni mkanganyiko wa hoja ninawajibika kuizijibu. (Makofi)

Mtu anakuambia, Mheshimiwa Mbunge anasema nchi inakufa hiyo kwenye CAG report haipo…

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Jesca Msambatavangu, Mheshimiwa Profesa Kitila, kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, nilikuwa naomba kwa kuwa wamesema wanajibu hoja nilikuwa naomba pia anajibu hoja kama Serikali anachangia whatever. Hizi anazosema trilioni mia na, zimehusiha na hizi za wizi ambazo CAG amezigundua na ambazo hatujazigundua, hizo trilioni. (Kicheko/ Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo unaipokea taarifa hiyo?

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ameuliza swali siyo taarifa, kwa hiyo, sihitaji kushughulika nayo hiyo.

Kwa hiyo, nilikuwa natoa mfano, nimetoa mifano miwili tu; mfano wa pili nyinyi wote mliopo Waheshimiwa Wabunge na sisi, ni nchi yetu. Sisi ni viongozi, mMtu anakuambia nchi inakufa hiyo katika political science unaongelea…

SPIKA: Mheshimiwa Profesa Mkumbo, kuna taarifa nyingine kutoka kwa Mheshimiwa Mpina.

TAARIFA

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, anajieleza vizuri kwamba amefanya financial analysis kwamba trilioni 280 haziwezi kupigwa. Sasa yeye katika financial analysis yake anajua zimepigwa ngapi? (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, naona taarifa zenu zinatoka kwa sura ya maswali ambayo Mheshimiwa Waziri kwa kweli halazimiki kujibu, kwa sababu ili Serikali iweze kujibu maswali ni katika kipindi cha maswali na majibu. Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, nirudie tena hoja lazima iwe na mantiki, fedha zote za nchi hii kwa taarifa ya mwaka jana ni trilioni 141. Mantiki inakataa kwamba zimeibwa trilioni 280, ni logic ya kawaida. Mantiki inakataa. Ya tatu…(Makofi)

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hiyo ni taarifa ya ngapi?

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, naomba ya mwisho.

SPIKA: Haya, Mheshimiwa Mtaturu, taarifa.

TAARIFA

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nimefurahi sana kaka yangu Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo ni Waziri wa Mipango. Naomba tu nimpe taarifa, kwamba miongoni mwa Taarifa ya CAG mambo yaliyojitokeza makubwa ya upotevu wa fedha ni pamoja na kuzima POS zaidi ya siku 1000. Yeye kama Waziri wa Mipango, tunaomba jibu namna gani Serikali itachukua hatua kwa zile POS zilizozimwa?

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, hiyo ilikuwa ni taarifa ya mwisho kwa Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, malizia mchango wako.

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, mfano wa pili, sisi ni viongozi we must be responsible. Mtu anakuambia nchi inakufa, hiyo kwenye political science maana yake failed state, siyo kweli. Unasemaje nchi inakufa inayojenga reli yenye kilometa 2600 kutoka Dar es Salaam hadi Kalema? Unasemaje nchi inakufa iliyotoa Rais wa IPU duniani how? Nchi ambayo dunia nzima imeiamini ikakubali kutoa Spika, inakufa vipi? Nonsense. (Makofi)

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mwongozo wa Spika.

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, ndio nasema pale ambapo hoja haina mantiki kama Waziri wa Serikali ya Rais Samia lazima nijibu.

Mheshimiwa Spika, haya niendelee nichangia kidogo kwenye CAG Report. Ukweli ni kwamba kisaikolojia macho ya binadamu yameumbwa kuona mabaya kuliko mazuri, ni kisaikolojia, lakini ndani ya CAG Report ameonesha yeye mwenyewe kwamba hatua kadhaa zimepigwa kwenye kutekeleza mapendekezo yake naomba ninukuu vipengele vinne muda ukiniruhusu.

Mheshimiwa Spika, kwenye Taarifa ya Ripoti ya Mwaka ya Miradi ya Maendeleo Utendaji wa Kifedha, ukurasa wa pili, CAG anasema; “zaidi ya asilimia 90 ya miradi ilipata hati zinazoridhisha kwa miaka mitano mfululizo kuanzia mwaka 2017/2018. Hii ikiwa ni ishara nzuri kwenye matumizi ya fedha na utendaji wa Serikali.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa wa pili, naomba nirejee tena alisema nini kuhusu Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, kwa sababu hoja imekuja hapa kwamba mradi umechelewa alisema nini. CAG anasema na nanukuu; “Nilibaini makadirio ya muda wakumalisjha mradi usio halisi, kwani mradi ulipangwa kumilika katika kipindi cha miaka mitatu, huku miradi ya ukubwa kama huo iliyojengwa duniani huchukua kati ya miaka minne hadi miaka kumi kukamilika, makadiro ya awali hayakuwa halisi.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii maana yake ni nini, maana yake ni kwamba wataalamu walitoa mapendekezo yao, lakini kuna mtu akatumia maamuzi ya kisiasa akaweka mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuchelewa kwa mradi siyo kwa sababu ya fedha…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, mfano wa tatu CAG…

SPIKA: Mheshimiwa, Sekunde 30, malizia.

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, mfano wa tatu, CAG kwa miaka mitano mfululizo amelalamika juu ya deni la TANESCO na TPDC. CAG akatoa mapendekezo kwamba Serikali iyageuze madeni haya na kuyasafisha vitabu vya mashirika. Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia miaka mitano imekubali na imetekeleza na CAG amesema pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano wa nne CAG alitoa mapendekezo kwamba Serikali ilipe madeni PSSF kiasi cha trilioni mbili kupitia Hati Fungani, Serikali imelipa na CAG amesema. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa. Muda wako umekwishwa.

WAZIRI WA MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Spika, umeisha? (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii. Nianze kwa kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao kwenye Sekta ya Viwanda na Biashara ambayo kwa kweli ilikuwa mingi na imekuwa hivyo kwa sababu Mpango wenyewe kwa kweli ukiangalia malengo 12 ya Mpango wa Maendeleo ambao tumeujadili hapa, malengo sita yanahusu Sekta ya Viwanda na Biashara. Mule ndani kuna hatua 116 za kiutekelezaji. Zaidi ya theluthi moja tu, 54 zinahusu Sekta ya Viwanda na Biashara. Kwa hiyo, naelewa kwa nini michango imekuwa mingi.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu ya muda, naomba nichangie tu jambo kubwa ambalo limejitokeza, ambalo nawe umelisisitiza; na nipanue pale Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji alipoishia kuhusu suala la utekelezaji wa Mpango wa Kuboresha Mfumo wa Udhibiti wa Biashara, maarufu kama Blueprint, ambao unalenga kuimarisha na kuboresha mazingira ya biashara na uwekezaji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu, kwenye mpango huo kuliibuliwa changamoto nyingi ambazo zinakwamisha mazingira ya biashara na uwekezaji, lakini unaweza kuzigawa changamoto hizo katika maeneo 11 ambayo tunayafanyia kazi. Ningetaka kuleta taarifa kwenye baadhi ya maeneo ili kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge. Nataka nitolee taarifa maeneo manne ambayo ni ya msingi sana. Moja sitalizungumza kwa sababu Mheshimiwa Mwambe ameshalieleza kuhusu suala la tozo, ada na adhabu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kama unavyofahamu, kwenye mpango huu iliainishwa kwamba tozo 45 ziliainishwa kama ni tozo za kero; na ziondoke; na zilifutwa. Ukiacha hiyo, tulienda mbali zaidi, zimefutwa jumla ya tozo 273 kama ambavyo Mheshimiwa Mwambe ameeleza. Kwa hiyo, ni hatua kubwa na hii ilikuwa ni moja ya kero kubwa sana ambayo iliainishwa kwenye changamoto za kufanya biashara.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, ilikuwa eneo la utungaji wa sheria na uboreshaji wa sheria na kanuni mbalimbali. Hapa zilitambuliwa sheria na kanuni 90 ambazo zinakwamisha mazingira ya biashara na uwekezaji. Tayari sheria na kanuni 11 zimefanyiwa kazi, pia tumeweka misingi 10 ya kuzingatia katika kuboresha sheria hizo.

Mheshimiwa Spika, kama baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wanavyofahamu, baadaye ilikuja kuonekana kwamba kuna haja ya kuwa na sheria moja ambayo ni kubwa, inayozungumzia biashara. Kwa hiyo, tuko katika mchakato ndani ya Serikali kuja na Muswada wa sheria ambao kwa sasa unaitwa Business Facilitation Act ambao utajibu changamoto nyingi za Sheria ambazo ziliainishwa hapa.

Mheshimiwa Spika, suala la tatu lilikuwa ni kuweka mfumo wa electronic. Hapa Waheshimiwa Wabunge wengi wanafahamu kwamba, ndani ya Serikali mifumo mingi ya electronic imeanzishwa kutokana na utekelezaji wa mipango hii ikiwemo GePG, BRELA, TBS, TIC, TMDA, kokote kule kwa sasa wanatumia mifumo. Wengi wanafahamu ukitaka sasa hivi kusajili Kampuni, huhitaji kwenda physically kwenye ofisi, una log in tu kwenye mfumo.

Mheshimiwa Spika, ya nne na hii ni kubwa ni suala la uanzishwaji wa vituo vya pamoja vya kutoa huduma. Vimeanzishwa ndani ya TIC, EPZA na mipakani. Nitoe taarifa pia hapa kwamba hatua inayofuata ni kuanzisha vituo vya kutolea huduma, yaani One Stop Service Delivery Center kwenye ngazi ya Halmashauri. Bahati nzuri tayari tumepata grant kutoka Umoja wa Ulaya Euro million 9.5. Hizi zinakwenda kujenga vituo vya One Stop Center kwenye ngazi za Halmashauri ili sasa kuja kwenye Halmashauri, badala ya mtu kwenda TRA, BRELLA na TBS, anaenda sehemu moja, anapata huduma zote kwa wakati mmoja. Tunaamini hili litakuwa ni mkombozi mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka tu niseme kwamba utekelezaji wa Blueprint unaendelea vizuri, tutakachofanya ni kuimarisha utoaji wa taarifa, nasi ambao tumeteuliwa na Mheshimiwa Rais hivi karibuni, tutaongeza kasi zaidi ili kuona kwamba, utekelezaji unakwenda vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nitoe taarifa, ilitolewa hoja hapa kwamba viwanda vyetu vya mafuta vinavyo tu single refinery. Hii siyo kweli. Ninayo orodha hapa ya zaidi ya viwanda 20 ambavyo finafanya double refinery. Nami nataka kushauri Waheshimiwa Wabunge, Wazungu wanasema, extra ordinary claim, demands extra ordinary evidence.

Mheshimiwa Spika, sasa ukitoa hapa claim ambazo ni kubwa, kwa sababu inataka kuonekana kana kwamba Tanzania mafuta ambayo tunatumia kule hayana ubora unaostahili, hapana. Mafuta yetu inajulikana kwa vipimo vyote kwamba ni mafuta bora sana ambayo tunazalisha hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilitaka kulitolea maelezo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, ni miradi ya kielelezo ambayo imetajwa hapa Mradi wa Chuma cha Linganga na Makaa ya Mawe ya Mchuchuma. Nataka tu niseme mradi huu ni miongoni mwa miradi 17 ambayo ipo katika miradi ya kielelezo na kwa kweli ambacho kilichochelewesha na nilitolea taarifa mwezi Februari ni kwamba tutaleta taarifa kamili katika Mpango…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: …na katika bajeti ambayo tutakuja nayo mwezi Mei.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianze kwa kukushukuru wewe na wasaidizi wako kwa maana ya Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mussa Zungu, Mheshimiwa Najma Murtaza Giga Mwenyekiti wa Bunge na Mheshimiwa Daniel Baran Sillo Mwenyekiti wa Bunge, kwa jinsi mlivyoendesha mjadala huu kwa umakini na uwazi wa hali ya juu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudia tena kuwashukuru Kamati ya Kuumu ya Bunge ya Bajeti, kwa uchambuzi wao makini na jinsi walivyoibua maeneo mapya katika mapendekezo ya Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote na hususani Wabunge takribani 116 waliopata nafasi ya kuchangia kwa kuongea ndani ya ukumbi huu, kwa maandishi na wale ambao walitoa taarifa. Nilikuwa nahesabu katika mjadala huu kulikuwa na Taarifa 29 na yenyewe ni michango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli binafsi hizi siku tano nilikuwa darasani. Nimejifunza mengi na kubainisha vema zaidi kuhusu kile ambacho watanzania kupitia Waheshimiwa Wabunge, wanataka kutoka kwa Rais wao, Serikali yao na nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unafahamu mimi ni mwalimu. Lazima nikiri kwamba, kupitia mjadala huu nillikuwa nafahamu lakini nimefahamu zaidi kwamba, una Wabunge makini sana. Una wabunge mahiri sana na humu ndani kumesheheni kila aina ya utaalamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana haujawahi kutoa takwimu, jana nilikuwa nafanya uchambuzi kidogo. Nadhani sasa Watanzania wajue kuwa Bunge hili ni tofauti sana. Limejaa watu wenye weledi tofauti na elimu zao ni elimu nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikusudii kujibu hoja za Waheshimiwa Wabunge katika hatua hii. Kwa sababu kwa kweli kazi yetu leo kama Serikali ilikuwa ni kusikiliza na kupokea ushauri na maoni ya Waheshimiwa Wabunge ambayo tumefanya. Kwa hiyo, sikusudii kujibu hoja moja moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli katika mjadala huu sisi kama Serikali tumeweza kubaini vipaumbele vya nchi yetu. tulikuja navyo lakini kupitia michango ya Waheshimiwa Wabunge unaweza ukaona kabisa watanzania wanataka vipaumbele gani. Naomba nikupe takwimu zifuatazo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika uchangiaji huu mpaka jana, Waheshimiwa Wabunge wameongelea mambo 307. Katika mambo haya mgawanyiko wake ni kama ifuatavyo: -

(i) Miundombinu ya usafirishaji ndiyo inayoongoza. Imeongelewa mara 68 kama asilimia 22.

(ii) Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Sekta hii imeongelewa mara 65.

(iii) Nishati imeongelewa mara 36.

(iv) Utalii na Hifadhi mara 38.

(v) Viwanda, Mara 33.

(vi) Biashara na Uwekezaji, mara 25.

(vii) Sekta binafsi, mara 12.

(viii) Afya, Elimu na mengine, mara 30. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, unaweza ukaelewa kwamba, kimsingi katika mipango yetu kwa vyovyote vile lazima tuzingatie maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mjadala wetu tumeendelea pia kubaini baadhi ya kero za wananchi. Tumezipokea na tutazizingatia. Kwa kipekee naomba niwambie wananchi wa Mbalali kwamba, kupitia Mbunge wao makini Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, tumewasikia. Aidha, tumewasikia wananchi wote wanaoishi karibu na hifadhi mbalimbali nchini. Kwa niaba ya Mheshimiwa Rais na viongozi wetu wengine wakuu na kwa niaba ya Waheshimiwa Mawaziri wenzangu, niwaeleze wananchi kwamba, Rais wetu anathamini maendeleo ya watu kuliko chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila kitu tunachokifanya nia na lengo letu ni hatimaye mwananchi mmoja mmoja, Jamii na nchi yetu kwa ujumla inufaike. Hii ni Serikali ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan. Pamoja na sifa nyingine, Rais wetu ni muungwana na mpenda haki. Rais wetu ni Mama mwenye huruma na mapenzi kwa watu wake. Rais wetu ni mwadilifu na mzalendo. Maelekezo yake kwetu ni kwamba, tuwatumikie wananchi na siyo kuwaumiza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya yote, hii ni Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. Kwa asili yake, panapotokea mgongano kati ya maendeleo ya Vitu, utu na maisha ya watu, CCM siku zote hukaa upande wa utu na Maisha ya watu. Naomba nirudie, zaidi ya yote hii ni Serikali ya CCM, kwa asili yake, panapotokea mgongano kati ya maendeleo ya vitu, utu na maisha ya watu, siku zote CCM hukaa upande wa utu na maisha ya watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunao mwongozo, na katika jambo hili tutakaa na kujipanga ili kuona kwamba Hifadhi zetu haziwi kikwazo au kugeuka mateso kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hifadhi zetu lazima zithamini maisha ya wananchi ili wananchi wazithamini. Tutajipanga na tutakuja na jibu endelevu katika suala hili. Hata hivyo, lazima pia tuombe Waheshimiwa Wabunge na wananchi kwamba, nchi yetu tayari tumekwishaamua kwamba, ni nchi itakayoongozwa kwa mujibu wa utawala wa Sheria. Tuombe sote tuzingatie Sheria, kama kuna Sheria zina shida ndiyo maana Bunge linakaa kila siku, tuje tubadilishe ili Sheria zitutumikie na siyo sisi kuzitumikia Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mjadala huu Waheshimiwa Wabunge wamebainisha na kusisitiza baadhi ya maeneo mapya ya kipaumbele ambayo kwa kweli katika mpango ama hayakuweko ama hatukuyapatia uzito wa kutosha, tutayazingatia. Mambo haya ni pamoja na yafuatayo: -

(i) Artificial intelligence, naomba nitamke hivyo kwa sababu wataalamu wa Kiswahili bado hawajawa na jibu sahihi la what is artificial intelligence in Kiswahili?

(ii) Uchumi wa gesi.

(iii) Fursa za kijiografia kwenye kutafuta maendeleo.

(iv) Fursa za mabadiliko ya Tabia ya nchi hasa suala la hewa ya ukaa.

(v) Haja ya kuanzisha mamlaka ya ufugaji na uvuvi, hili limejitokeza. Pia, kwa kweli katika nchi yetu karibu kila sekta ina chombo kinachoisimamia. Hata hivyo, suala la ufugaji na uvuvi nadhani ni eneo la kuliangalia kwa umakini sana.

(vi) Imejitokeza haja ya kuanzisha mamlaka ya maendeleo vijijini. Haya ni mambo ambayo tutayaangalia na kuyazingatia katika kuandaa Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kusisitiza na kutolea ufafanuzi kidogo kwenye maeneo mawili anbayo yamesisitizwa sana na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni maendeleo vijijini na nashukuru na kufurahi kuona kwamba Waheshimiwa Wabunge wameunga mkono na kuweka uzito mkubwa katika eneo hili. Kimsingi tayari tunao msingi wa maendeleo vijijini yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia TARURA mtandao wa barabara vijijini umongezeka sana katika miaka ya hivi karibuni; kupitia REA vijiji vingi sana vina umeme, kupitia RUWASA huduma ya maji imeendelea kusambazwa. Aidha, huduma za Afya na Elimu zinazidi kusambaa katika vijiji vyote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, watu wetu wakishakuwa na afya, wakapatiwa elimu, wakapata maji na umeme na wakaunganishwa katika mtandano wa barabara, tunahitaji kutumia yote haya kama nyenzo ya kuchochea uzalishaji ili hatimaye wananchi wetu huko vijijini wapate fursa za kiuchumi na kutengeneza vipato. Ndiyo nia yetu ya kusisitiza umuhimu wa kuvutia uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo vijijini kwa ajili ya kufanya primary processing. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, umuhimu wa kujenga muafaka wa kitaifa. Wataalamu wa maendeleo wanakubaliana kwamba, moja ya kikwazo cha maendeleo katika nchi yoyote ile, ni pale ambapo panakuwa hakuna muafaka kuhusu Mpango na vipaumbele vya maendeleo miongoni mwa wananchi na hususani watu wenye sauti katika jamii, wakiwemo viongozi wa makundi mbalimbali, wasomi, wafanyabiashara, wanasiasa nakadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana ni muhimu sana kushirikishana ili tukubaliane sote. Tukubaliane tunakwenda wapi? Kama ni kubishana tubishane njia ya kwenda, kama safari yetu ni Mwanza wote tuelekee Mwanza. Mwingine aseme nakwenda kwa gari, ndege, helikopta nakadhalika lakini tunakwenda wapi? Tuwe na mwelekeo mmoja ni jambo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe kwa kujibu swali moja ambalo Waheshimiwa Wabunge wameliuliza na lenyewe je, nilipozungumizia kwenye hotuba yangu nilizungumzia umuhimu wa kuwa na watu wazuri kwenye Serikali. Pia, Waheshimiwa Wabunge wameuliza, je, tuna watu wazuri katika utumishi wetu wa umma? Jibu langu ni ndiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaposema ndiyo, narejea na ninaangalia walimu zaidi ya 250,000 ambao wanafundisha na kulea watoto wetu sisi tukiwa hapa. Ninapozungumzia watu wazuri, ninazungumzia zaidi ya madakatari na manesi zaidi ya 48,000 wanaotibu watu wetu katika zahanati na vituo vyetu vya afya kwa kiwango ambacho leo Tanzania ndiyo nchi yenye vifo vichache vya wakinamama kusini mwa jangwa la Sahara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumzia zaidi ya mafundi 9,000 ambao wanasambaza maji vijijini. Ninazingatia uadilifu, uzalendo na umakini wa Rais wangu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, pamoja na Baraza lake la Mawaziri. Ninazungumzia umakini wa viongozi wangu wakuu, Mheshimiwa Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu na kwingine. Of course, ninapouzungumzia kwamba tunao, ninazungumzia umakini, uzalendo na umahiri wa Spika wangu Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, wote hawani watu wema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunachopaswa kufanya ni kuimarisha mifumo yetu ya uwajibikaji na kuendelea kujenga uwezo wa watu wetu kwenye utumishi wa umma. Hatuwezi kukata mwembe wote kwa sababu ya kuoza kwa maembe mawili. Tuyaondoe maembe mawili yaliooza lakini lazima mwembe ubaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamalizia kwa kusema, ninakubaliana na Waheshimiwa Wabunge kuhusu umuhimu wa kuzingatia maadili kwa watoto wetu. Hata hivyo, tunapoendelea kuelimisha vijana wetu kuhusu maadili, tusije tukawaondolea haki yao ya kuwa watoto. Ni muhimu watoto wakabaki kuwa watoto, kwa sababu bila hivyo watakuja kufanya utoto wakiwa watu wazima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuzingatie kuwa utoto wa watoto wetu hauwezi kuwa utoto ulivyokuwa utoto wetu sisi. Utoto wa watoto wetu mazingira ni tofauti na tukitaka wawe kama tulivyokuwa sisi, tutakuwa tunawakosea. Tuache watoto wawe watoto, tuwape maadili lakini ni muhimu wawe watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo niseme tena kuwa, sisi kama Serikali tumepokea maoni na ushauri wa Waheshimiwa Wabunge na tutayazingatia katika kuandaa Mpango wa Maendeleo ujao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsanteni sana kwa fursa hii. Mungu ibariki Tanzania, Mungu ibariki Afrika. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii, naomba nichangie mambo manne kama muda ukiniruhusu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwanza ni umuhimu wa bajeti umuhimu wa hotuba ya hali ya uchumi, ni hotuba muhimu sana kwa sababu ndiyo inayotuonesha uwezo wetu wa kiuchumi na uwezo wetu wa mapato ili tunapopanga matumizi tujue nguvu yetu iko wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ndiyo hotuba ambayo inatupa vipaumbele vya Kitaifa, changamoto tu ni kwamba Waziri wa Mipango ndiye huyo huyo ni Waziri wa Fedha, kawaida Waziri wa Fedha ana mambo mengi ndiyo maana kitabu chake ni kikubwa wakati ile hotuba ya mipango ni kidogo, kwa sababu ina concentrate na mambo machache. Waziri wa Fedha anataka ikiwezekana fedha zote za nje ziingie Serikalini, yaani fedha zote katika nchi hii awe nazo yeye na ikiwezekana mahitaji yote ayamalize leo, ndiyo maana utaona ikisomwa humu ndani kuna mambo mengi unasoma unakutana na kiswahili kitumike kwenye usaili, unaelewa ni jambo jema kubwa na tukalipigia na makofi ni jambo zuri, lakini yote hii ni kwa sababu Waziri wa Fedha ana mambo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, of course nilikuwa nasoma nikasema dhima yetu ya mpango wetu wa maendeleo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya watu, nadhani kisera ni muhimu kuwasisitiza watoto wa Kitanzania na Watanzania ili waweze kushindana, wajue vizuri Kiswahili, wajue vizuri Kiingereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshakubaliana hapa tena Waziri anafahamu, tumeshafungua soko la ajira free movement of labor, sasa watakapoenda kule Uganda kufanya interview watu wetu inabidi na wenyewe washindane kwa hiyo, hili ni muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na hiyo changamoto ushauri ni kwamba pengine Bunge hili linaweza likaishauri mamlaka lione umuhimu tena wa kutenganisha hizi sekta mbili, za mipango na fedha. Nadhani tulipoandaa ile dira yetu ya mwaka 2025 ukiisoma ndiyo maana aliyesaini pale, hakusaini Waziri wa Fedha wakati huo Mheshimiwa Daniel Yona alisaini Mheshimiwa Nassor Malocho aliyekuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Mipango, nadhani hili kuna haja ya kulifikiria tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge letu tujielekeze wenyewe na kujishauri pengine kuna haja hii hotuba ya hali ya uchumi ikatolewa mapema kabla sekta hazijaanza kuwasilisha bajeti, ili sasa wanavyokuja kuwasilisha bajeti za kisekta tuone hizo sekta ambazo zinawasilishwa kama zinaendana na hali yetu ya uchumi na vipaumbele ambavyo tunavyo and then, siku hii saa kumi ije bajeti ya National Budget ndiyo tuipokee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni kodi. Katika eneo la kodi nataka nianze kwanza kuwapongeza wafanyakazi wa Tanzania wanaoiongoza nchi hii siyo kwenye utumishi tu, lakini pia kwenye suala la mapato. Ukisoma takwimu za TRA wafanyakazi wa Tanzania ndiyo wanaoongoza kulipa income taxes, wanawazidi business income tax, wanawazidi mpaka cooperation tax, yaani ile tunayosema large tax payers hawawafikii wafanyakazi wa Tanzania. Wafanyakazi wa nchi hii wanalipa, ukisoma zile takwimu 12.3 percent ya makusanyo yote ya TRA ni pay as you earn, wafanyakazi wa Tanzania ukisoma zile za juzi 2.2 trillion shillings kutoka kwa wafanyakazi. Wafanyakazi wa nchi hii waheshimiwe, wanafanyakazi kubwa, tunawashukuru sana kwa mchango ambao wanaoutoa katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa pongezi vilevile kwanza kwa Mkoa wa Dar es Salaam, ukisoma takwimu za TRA asilimia 79 ya makusanyo yote ya kodi yamekusanywa kupitia Dar es Salaam, Dar es Salaam is the largest tax collection center in the country. Tunazungumzia Trilioni 13.9 kati ya Trilioni 17.6 ahsanteni sana Mkoa wa Dar es Salaam. Pia ukiangalia kwa maana ya wananchi wanaolipa kodi, asilimia 11 ya kodi zote za nchi hii zinalipwa na Mikoa Mitatu ya kikodi kwa maana ya Ilala, Kinondoni na Temeke of course kwenye Kinondoni pia pale Ubungo ipo, usisahau Ubungo ipo ndani ya Kinondoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hawa tunaozungumzia Trilioni 1.996, Mikoa mingine yote ukijumlisha wanalipa kodi Trilioni 1.921. Kwa hiyo, makusanyo ya Mikoa Mitatu ya kikodi Dar es Salaam inazidi Mikoa yote ya Tanzania ukijumlisha. Wananchi wa Dar es Salaam shikamooni sana, tunawashukuru sana kwa kuchangia. Nataka niwaambie shukrani za Serikali ya CCM….

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Stella Manyanya.

T A A R I F A

MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza namshukuru Profesa kwa mchango mzuri lakini naomba nimpe taarifa moja, sisi ambao tunatoka kwenye maeneo yasiyolipa kodi kiasi hicho siyo kwamba hatutaki, lakini uwekezaji mkubwa umefanyika kwenye maeneo hayo na lazima mlipe hizo kodi, ndiyo maana tunaomba sasa nchi, Serikali iangalie na maeneo mengine ili na sisi tuweze kuchangia kwa kiasi hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo unaipokea hiyo taarifa?

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siwezi kukataa taarifa ya Dada yangu naipokea tu hata kama siijui sana, hiyo naipokea haina matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, point yangu ni hapo hapo kwamba nataka nichukue nafasi hii kuwahakikishia wananchi wa Mkoa wa Dar es Salaam Serikali ya Chama cha Mapinduzi hii

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo Chief Whip anataka kuzungumza.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza mimi ni shabiki wa kusikiliza michango ya Profesa, ili tuweke mambo sawasawa hapa, hizi trilioni 13.9 zilizokusanywa na Dar es Salaam, Da es Salaam siyo wazalishaji, wanaozalisha wapo Mikoani, ndiyo maana asilimia 90 ya magari yetu ya mizigo, yote yametizama Dar es Salaam, tukiziba hizi barabara Dar es Salaam mtakufa njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo wamezalisha Dodoma, wamezalisha Mikoa yote nilitaka kumpa taarifa tu hiyo ili Watanzania wengine wasije wakajiona hawa mchango kwa nchi yao.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo unaipokea taarifa?

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Taarifa yake haina shida naipokea, mambo ya kuzingatia ni mawili nimeweka takwimu mbili na naomba unitunzie muda wangu, takwimu mbili za msingi za kuzingatia. Dar es Salaam kama collection center ndiyo hiyo Trilioni 13.9, hizo maana yake Watanzania wote wamechangia, ikiwemo airport, ikiwemo bandari, ile ni bandari ya wananchi wote wa Tanzania, kwa hiyo, hiyo ni Watanzania wote mpaka wa Singida na Iramba wamechangia hilo halina shaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna takwimu ya pili ambayo ni shukrani kwa Mkoa wa Dar es Salaam ni wananchi ambao wamechangia 1.996 trillion wananchi wa Ilala, Kinondoni na Temeke, hawa ndiyo nawalinganisha na wengine. Sawa hawa Mheshimiwa Waziri hawa watatu hawa, wamekusanya kuliko nchi nzima ukijumlisha, wanastahili shukrani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo, nataka niwahakikishie wananchi wa Dar es Salaam kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi zile ahadi zake za kujenga barabara za mitaani itatekeleza ili mkusanye zaidi fedha. Nataka niwaambie Tarehe 31 Mei mwaka 2022, Mawaziri watatu walikutana na Wabunge Wabunge wa Dar es Salaam wakiongozwa na Waziri wa Fedha Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, pamoja na Waziri wa Ujenzi na wametuhakikishia kwamba mradi wa DMDP upo, zile barabara zitajengwa na akitoa ahadi Mnyiramba huwa havunji, kwa hiyo hili litakwenda vizuri.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu, nataka nipongeze TRA kwa kazi nzuri. Sisi tumekaa hapa tunachangia vizuri kwa sababu kuna watu wamekusanya mapato tukalipwa ambavyo tunalipwa na utaratibu wetu ukakamilika, TRA ahsanteni sana. Pamoja na hayo wameshasema Waheshimiwa Wabunge hapa tunachangamoto kwa kweli, bado tunakusanya kidogo sana! Kwa hapa East Africa sisi ndiyo tuko chini, wote tumewazidi DRC tu ambao wamejiunga juzi, lakini mpaka Burundi wametuzidi hii ni changamoto. Tunakusanya only 4.5 percent ya walipa kodi Tanzania. 2.7 Million out of Six Billion, only 4.5 percent ya watu wote wanaolipa kodi. Kwa kweli ni jambo ambalo linasikitisha lazima tutoke hapo, tusonge mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri, bahati nzuri TRA wamewahi kufanya study, TRA ilikuwa na maboresho katika maeneo mawili, eneo la kwanza ilikuwa ni hili kuitoa TRA kuwa chombo cha utawala kwenda kuwa component tax ya TRA. Eneo la pili ilikuwa waende kwenye ku-improve efficiency na walikuwa na mambo kadhaa, moja kupunguza viwango vya kodi, kurahisisha ulipaji kodi, wakaja na mapendekezo mengi lakini moja ya pendekezo zuri sana ilikuwa ni kwamba tupunguze wigo wa VAT iwe kati ya asilimia 10 mpaka 20, halafu tupunguze utiriri wa kodi kwenye Local Government Authority, badala yake VAT inayokusanywa watakuwa wengi wakishaongezeka, Serikali Kuu ibaki na asilimia 75 halafu Local Government Authority ibaki na asilimia 25 ya VAT, hivyo tutakuwa tumesaidia sana kwa maana ya accumulation wa zile kodi ni za kwetu lakini pia kupunguza utitiri wa kodi katika maeneo ya Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu Dar es Salaam nimerudia tena hapo, nilishatoa hapa angalizo na nikasisitiza Majiji yote yana sifa Kumi, lakini kwa sababu ya muda nitaje mbili. Moja miundombinu nadhifu ya usafiri, hii ni muhimu na ninaipongeza Serikali kwa kujenga Daraja la Tanzanite, sasa Mheshimiwa Waziri tumejenga daraja lile zuri kwa mkopo halafu unakuja na tozo achana na hiyo biashara. Daraja la Tanzanite ni daraja zuri, lilijengwa kwa lengo la kupunguza foleni katika hii barabara ya Ali Hassan Mwinyi na ni daraja zuri, kwa hiyo usiharibu furaha ya Dar es Salaam kwa kuweka tozo, achana na hiyo biashara.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kuna kitu kinaitwa 24 hours activity, Majiji yote yanakuwa na ‘K’ tatu, piga kazi masaa 24, kula maisha masaa 24, lipa kodi masaa 24, Mheshimiwa Waziri hawa watu ndiyo wanakulipa kodi, habari za kusema fungua biashara kuanzia Saa Sita, achana na hiyo kitu! Eti, Jumamosi unaambiwa kwamba msifungue biashara mpaka usafi ufanyike, mambo ya wapi hayo? Hayo mambo hayawezi kuwa katika Majiji Mheshimiwa Waziri, kwenye hotuba yako umesema sanaa na burudani ndiyo inayokuwa kwa kasi kiuchumi, sasa burudani makao makuu yake si Dar es Salaam? achia Dar es Salaam 24 hours. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni ushauri. Mheshimiwa Waziri umeongeza import duty kwenye cotton yarn, Tanzania bahati mbaya Waziri wa Kilimo hayupo, hapa tuna ginnery peke yake hatuna spinning ukiongeza cotton yarn itabidi ufunge viwanda vya A to Z utafunga NIDA, utafunga kama viwanda vitano hivi, kwa sababu hapa hatuna raw materials. Hili jambo tumelizungumza mwaka jana, ninaomba sana Kamati ya Bajeti na wewe Mheshimiwa Waziri mliangalie, kwa kuweka import duty 24 percent mpaka 35 percent hatutaweza kushindana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, duniani cotton yarn viwanda viko vichache mno ambavyo vinazalisha vingi tuna-import, sisi shida yetu tunataka tupate agro-processing industry tusafirishe mazao ambayo yamechakatwa, kwa hiyo kuleta yarn hapa ni jambo jema naomba sana liangaliwe hili ili viwanda vyetu visije vikaathirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kukushukuru sana kwa jinsi ambavyo umeendesha mjadala huu na kutupa nafasi ya kuweza kuwasilisha Azimio hili. Nimshukuru sana Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuruhusu Mkataba huu uwasilishwe hapa Bungeni kupitia Baraza lake la Mawaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nichukue nafasi hii pia kumshukuru sana Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira, Mheshimiwa David Kihenzile na Makamu wake Mheshimiwa Eric Shigongo na Wajumbe wote kwa nafasi ambayo walipata ya kuchambua kwa kina sana Mkataba huu. Nikutaarifu tu kwamba siku tunajadili Mkataba huu, tulikuwa na Wenyeviti wa Kamati wengine walikuja kushiriki zaidi ya Wenyeviti watano. Kwa hivyo, siku ile ilikuwa ni mjadala mzuri sana na Waheshimiwa walipata nafasi ya kuchambua na kuuliza maswali na sisi ni wataalamu tuliweza kuwajibu ipasavyo. Pia nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamepata nafasi ya kuchangia, kwa hoja zao lakini pia kwa uwingi wao na ujumla wao kwa kuunga mkono hoja hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kwa kiasi kikubwa karibu Wajumbe wote wameunga mkono hoja hii, sitaki kutumia nafasi hii kuchukua muda wako mwingi katika kujibu. Naomba nitoe ufafanuzi kwa maeneo machache sana katika kuhitimisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kutoka kwa Kamati walitoa maoni na mapendekezo kwamba ni muhimu sana tukachagua bidhaa za kulindwa kwa umakini mkubwa. Nataka tu nilitaarifu Bunge lako kwamba katika Mkataba huu na katika majadiliano ambayo tumeyafanya kwa sasa tumekamilisha majadiliano kwenye Itifaki tatu; Itifaki ya Biashara ya Bidhaa; na Itifaki ya Biashara ya Huduma na Utatuzi wa Migogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukubaliana huku tumegawa bidhaa katika makundi makubwa matatu. Kuna kundi la kwanza ambapo tunajadiliana tufikie asilimia 90 na Wakuu wa Nchi na Serikali waliagiza kwamba ili biashara ianze kufanyika tukubaliane kufanya biashara katika angalau asilimia 90 ya bidhaa. Sisi tuna-negotiate kama Afrika Mashariki na tumeshakubaliana asilimia 86, majadiliano yanaendelea ili tupate bidhaa tufike asilimia 90.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kundi la pili ni asilimia 7 ambazo hizi hatutaingia kwa sasa, tutaingia katika kipindi cha miaka 13 ijayo. Hizi ni bidhaa ambazo zitaingia katika soko hili baadaye katika miaka 13.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna kundi la tatu ambalo ni asilimia 3, hizi ni bidhaa ambazo hatutaingia kabisa. Hizi ni bidhaa ambazo nchi zimekubaliana zipo kwenye kitu kinaitwa exclusion list kwamba zenyewe hazitakuwa sehemu ya bidhaa ambazo zitafunguliwa masoko haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, wataalamu na Serikali tumekaa tayari tunaendelea na majadiliano kuona kwamba ni bidhaa gani ziingie kwenye asilimia 3, zipi ziingie kwenye asilimia 7 na zipi ambazo ziingie kwenye asilimia 90. Kwa hivyo, Serikali ipo makini kwenye jambo hili lakini pia Mkataba umetoa mawanda mapana kuhakikisha kwamba nchi zinalindwa katika hatua zake za viwanda na biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili, nataka tu niseme kwamba tayari sisi kama Tanzania tuna-advantage ukilinganisha na wenzetu kwa sababu sisi tayari tupo katika nchi 19, kwa maana ya kwamba sisi ni Wajumbe wa EAC na Wajumbe wa SADC, kwa hiyo, tayari tulishafunguliana masoko yetu. Kwa hivyo, sisi ni wazoefu wa kutosha, katika nchi zote 54 tayari sisi tunafanya biashara na nchi 19, kwa hivyo, hili jambo siyo jipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyosema wengine, tathmini imefanyika kwa kina sana na Wizara ya Fedha na Mipango kuona matokeo chanya na hasi ya kujiunga na Mkataba huu. Hitimisho ni kwamba matokeo chanya ni mengi zaidi na kwamba ni lazima twende kwenye Mkataba huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyosema wengine, nikitoa mfano tu takwimu za mwaka jana tumeuza EAC dola milioni 812 ukilinganisha na zile ambazo tumeingiza Tanzania dola za Kimarekani milioni 324. Kwa hivyo, tunauza zaidi kuliko vile ambavyo tunavyonunua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, SADC tumeuza dola za Kimarekani milioni 999 wakati ambazo tumenunua sisi ni dola za Kimarekani milioni 604. Kwa hivyo, hakuna kipya ni kwamba uzoefu tunao na kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge tunafanya vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingine niitolee ufafanuzi kuhusu hizi tozo, Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo kwamba lazima tufanye review na kuna review kubwa inaendelea kuhusu tozo mbalimbali jinsi ambavyo tunakamilisha biashara. Tunaamini kwamba mwaka huu tutapata suluhu kwa baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nieleze hili la ETS na VAT refund ambalo Mheshimiwa Mwanyika aliliongelea, kama ambavyo mnafahamu, tayari Serikali imeshaanza kulipa VAT refund. Sisi tumeshapokea pongezi nyingi kutoka kwa wafanyabiashara wakishukuru sana kitendo ambacho Serikali imefanya cha kuanza kuwalipa VAT refund. Pia ETS tunafanya majadiliano na Wizara ya Fedha na wafanyabiashara ili kuona kwamba gharama za huduma hii zinapungua, tumeshakubaliana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hoja nyingine ambayo ni ya msingi pia imetolewa na Waheshimiwa Wabunge kuhusu utafiti za kina na hili aliliongelea Mheshimiwa Aida juu ya faida na hasara. Kama nilivyosema Serikali imefanya utafiti wa kutosha sana lakini pia watafiti huru wameshiriki kwenye suala hili. Tunao utafiti wa REPOA na Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na wame-publish study mbili hapa muhimu kabisa na zote ni mpya za mwaka jana. Moja, inaitwa: “Cost and Benefits of Regional Integration in Tanzania: Case Study of African Continental Free Trade Area”. Hitimisho lao ni kwamba Tanzania ijiunge na eneo hili mapema sana kwa sababu kuna faida kubwa kuliko hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini study ya pili ambayo wameifanya inasema: “Regional Integration and Tanzania’s Export Performance” wakiifanyia EAC na SADC. Katika study yao wameonyesha wazi kwamba Tanzania katika miaka 10 iliyopita imekuwa ikifaidika sana kuwa Mjumbe wa EAC na Mwanachama wa SADC katika suala zima la biashara. Hitimisho lao ni kwamba hatuna sababu ya kuogopa, tujiunge haraka kwa sababu kwa kweli nchi inakwenda kufaidika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama walivyosema Waheshimiwa Wabunge hatuna sababu ya kuogopa. Tupo tayari na Serikali imefanya maandalizi ya kutosha sana kwa ajili ya kujiunga na eneo hili. Pia wafanyabiashara tumefanya nao kazi sambamba na kwa kweli wao wangetaka tujiunge juzi sio leo. Kwa mfano, hata leo asubuhi wameniandikia email kunitakia kila la kheri katika kuwasilisha Azimio hili na kuwaomba sana Waheshimiwa Wabunge waridhie. Kwa hiyo, napenda kusema kwamba Serikali imejiandaa, wafanyabiashara wamejiandaa na tupo tayari kufanya kazi na wenzetu katika eneo hili la biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nihitimishe kwa kusema kwamba nchi yetu iliongoza mapambano ya ukombozi wa kisiasa katika Bara la Afrika. Sisi ndio tulikuwa viranja, tunapoanza mapambano ya ukombozi wa kiuchumi hatuwezi kubaki nyuma. Mkataba huu unatupa fursa ya Tanzania kuchukua nafasi yake katika Bara la Afrika katika kuongoza mapambano ya kujikomboa kiuchumi. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge waridhie Azimio hili ili tuanze safari hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawasalimu kwa Jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba kutoa hoja. (Makofi)

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kwanza niungane na Mwenyekiti wa Kamati yetu, kupongeza sana juhudi za Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa ujenzi wa miundombinu ya shule na hasa madarasa yale ambayo tumeyapata. Katika Halmashauri ya Ubungo tumeweza kupata madarasa 151 ambayo yamesaidia sana kupunguza changamoto hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nataka nichangie kwa dakika ambazo ninazo, ni haja ya Serikali kushughulikia upotevu katika mfumo wetu wa elimu. Kuna upotevu mkubwa sana na nitatoa mifano mitatu. Mfano wa kwanza, wanafunzi waliofanya mtihani wa Form IV mwaka 2021, walianza shule ya msingi mwaka 2011. Walianza wakiwa 1,500,000; waliofanya juzi mwaka 2021 ni wanafunzi 483,820. Inamaanisha watoto 1,000,000 na zaidi wamepotea wakiwa na umri wa miaka 13.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa pili, katika wanafunzi waliofanya mtihani wa Kidato cha IV 483,820, katika nchi hii huwa tunapima ufaulu katika madaraja manne; daraja la kwanza, la pili, la tatu na la nne na la mwisho la kufeli. Daraja la nne huwa tunaita ufaulu hafifu. Kwa hiyo, kwa maana ya ufaulu proper, daraja la kwanza mpaka la tatu katika wanafunzi waliofanya mtihani huo, 483,820 waliofaulu daraja la kwanza mpaka la tatu ni wanafunzi 173,000 peke yake sawa sawa na 35.8%. Inamaanisha katika eneo hilo pia, watoto takribani 300,000 wamepotea. Kwa hiyo, mpaka unafika form four umeshapoteza watoto 1,300,000, zaidi ya 70%. Big wastage!

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano wa tatu, mwaka 2021 Ofisi ya Waziri Mkuu wamefanya utafiti mzuri sana, unaitwa utafiti wa nguvu kazi katika nchi yetu; na wakabaini kwamba Tanzania tuna watu milioni 33 hivi ambao ni nguvu kazi wanaoweza kufanya kazi ambao ni 54% ya population yetu. Katika hao, 16% ya nguvu kazi hiyo hawajawahi kwenda shule kabisa; 65% ndiyo Darasa la Saba na 15% ndiyo form four. Inamaanisha kwamba mpaka hapo 96% ya nguvukazi yetu ni nguvukazi ambayo imepita katika mfumo wa elimu bila stadi zozote za kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu ya ufundi, VETA hii ambayo tunaizungumzia, waliopita katika nguvukazi ni 1%; elimu ya juu ya kati ni 1% nyingine. Vyuo Vikuu ambavyo mnadhani tuko wengi sana, nguvu kazi yetu ni 2% peke yake. Kwa hiyo, ni 4% ya nguvukazi yetu unaweza ukasema angalau wamepita katika mfumo fulani wa stadi za kazi na maisha. Very big wastage Maana yake nini? Ni kwamba mfumo mfumo wetu wa elimu haujasambaa. Ni mfumo ambao uko vertical, ukishakosea sehemu moja, unatoka katika mfumo. Kwa hiyo, lazima tatizo hili kama Serikali tulione. Ushauri wangu, badala ya kushughulikia changamoto hizi nusu nusu, tuupitie na kuupanga upya mfumo wetu wa elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili siyo geni. Mwaka 1982, Rais wetu wa Kwanza Mwalimu Nyerere aliunda Tume ya Makweta, maarufu kama Makweta Commission ikaupitia mfumo wetu wa elimu. Ilifanya kazi zaidi ya mwaka mmoja, ikatoka na taarifa ambayo ilitusaidia kwa miaka 20. Ndiyo iliyotupa Sera ya Elimu na Mafunzo ya 1995. Sera ya elimu na mafunzo Mheshimiwa Waziri wa Elimu ya 2014 siyo product ya research yoyote; sera pekee ambayo ni product ya research ni ya 1995. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nashauri kwa bidii kwamba Waheshimiwa Mawaziri na Serikali tumshauri Mheshimiwa Rais akubali kuunda a Presidential Commission ambayo itapitia upya mfumo wetu wa elimu tupange upya. Jambo hili kugusa tu mtaala wa Primary na Sekondari, haiwezi kututoa. Tunahitaji elimu ambayo ita-fit katika karne ya 21 na ambayo itatupeleka miaka 20 mingine ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri dira yetu inaisha mwaka 2025, kwa hiyo, na hii itatupa nafasi ya kwenda sambamba na dira yetu ya mwaka 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nina maeneo mawili ya kuchangia katika hoja hii kama ifuatavyo: -

Kwanza, Serikali imalize mgogoro kati ya wananchi wa Mtaa wa Baruti na TANROADS.

Mheshimiwa Spika, kwa muda mrefu kumekuwepo na mgogoro kati ya wananchi wa Mtaa wa Baruti na TANROADS kufuatia uamuzi wa TANROADS kuwataka wananchi wapishe eneo la makazi yao kwa ajili ya upanuzi wa barabara husika. Madai ya muda mrefu ya TANROADS ni kuwa wengi wa wananchi hawa walishalipwa fidia. Hata hivyo wananchi wanapinga madai haya. Historia fupi ya mgogoro huu ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, miaka ya 1990 barabara hii ilikuwa na lanes mbili, moja ikiingia na moja ikitoka. Baadaye Serikali iliona haja ya kupanua barabara hii. Hivyo wananchi waliofuatwa na barabara walilipwa fidia na kupewa maeneo ya kujenga katika maeneo ya Mbweni na Mabwepande. Hii ndio asili ya Mtaa wa Ubungo kule Mbweni na Mtaa wa Manzese kule Mabwepande.

Mheshimiwa Spika, mgogoro uliopo kwa sasa ni pale Serikali ilipoamua kupanua tena barabara kuwa njia nne kwa kila upande. Katika hatua hii ndipo ilipowakuta wananchi. Hawa ni wananchi ambao wamekutwa na barabara inayopanuliwa na baadhi yao wameisha katika maeneo husika kwa zaidi ya miongo mitatu.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ardhi Na. 4 ya mwaka 1999 (hususani kifungu cha 3b) ipo wazi kwamba; katika hatua zozote za kuendeleza ardhi ni muhimu “kuhakikisha kuwa haki za wakazi waliokaa muda mrefu zinalindwa….”

Mheshimiwa Spika, ninaomba Serikali imalize mgogoro huu ili wananchi waishi kwa amani na kufanya shughuli za maendeleo na wakazi wa maeneo husika wapewe haki zao kwa kuzingatia sheria zilizopo.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali itekeleze ahadi ya muda mrefu ya kujenga barabara ya Kimara – Mavurunza – Kinyerezi.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana wakati wa mjadala wa Wizara hii mimi na Mbunge mwenzangu wa Jimbo la Segerea, Mheshimiwa Bonnah Kamoli, tulizungumza kwa sauti kubwa sana kuhusu umuhimu wa barabara ya Kimara -Mavurunza - Kinyerezi yenye urefu wa kilometa saba na ambayo ipo chini ya TANROADS, niliamini Waziri alituelewa, na tangu mwaka jana na mwaka huu tumezunguka ofisi zote husika, zikiwemo kwa CEO wa TANROADS na Katibu Mkuu wa Ujenzi, Engineer Aisha Salim. Aidha, tumezungumza na Waziri na Naibu Mawaziri mara nyingi. Wote hawa walituahidi kwamba mwaka huu barabara hii ingeingia katika bajeti na ingeanza kujengwa. Na kweli tumeona barabara katika randama. Lakini sasa ndio imetengewe shilingi bilioni moja kwa kilometa tatu?

Mheshimiwa Spika, tangu lini bilioni moja ikajenga kilometa tatu za lami? Halafu Waziri amezungumzia kufanya feasibility study. Hili ni jambo ambalo tuliambiwa lilishafanyika tayari, hatuwezi kueleweka kwa wananchi. Naomba Waziri atakapohitimisha hoja yake atueleze ni lini barabara hii itaanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. Nitasubiri majibu ya Mheshimiwa Waziri kabla sijaamua kuunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii Kuhusu Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu kutofuata Maelekezo ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kama Mjumbe wa Kamati niweze kuchangia. Kwanza naunga mkono taarifa hiyo, na nataka kuchangia ile sehemu ya mwisho.

Mheshimiwa Spika, msingi wa changamoto ambayo tumeijadili hapa leo na siku iliyopita; moja, ni ukweli kwamba Waheshimiwa Wabunge pengine kuna haja ya kubadilisha tafsiri ya suala la anayestahili na asiyestahili. Hili ni tatizo ambalo limeendelea kujitokeza; na tulipoongea na bodi walikuwa wazi sana, kwamba kwa kweli wanafunzi wengi wanaoomba mikopo ya elimu ya juu wanastahili kupata mikopo hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto ambayo ipo ni ukweli kwamba bajeti inakuwa haitoshi, ni kama sisi Waheshimiwa Wabunge tunapokwenda kugombea huko, wote wanaogombea wanastahili lakini sasa inabidi warudi watatu. Kwa hiyo, ni lazima utaratibu upatikane wapatikane watatu na hatimaye mmoja, lakini haimaanishi kwamba wale ambao hawakuteuliwa hawastahili.

Kwa hiyo, hata kwenye suala la mikopo tuliona kwa upana wake. Nitawapeni kidogo tathmini, Bodi ya Mikopo inapitia hatua tatu muhimu kabla haijatoa orodha. Kwanza inapokea majina ya watu waliomba, pili wanahakiki. Wakishahakiki wanachukua wale ambao wamepata udahili katika vyuo vikuu.

Mheshimiwa Spika, sasa katika mwaka 2021/2022 waliyoomba mikopo walikuwa 88,688, Bodi ikafanya uhakiki, waliokuwa na sifa zile ambazo bodi inazo wakawa 81,654. Hii ina maanisha kwamba kwa vigezo vya Bodi hawa wote walistahili kupata mikopo. Hata hivyo baadaye waliokuwa wamekidhi vigezo vya udahili katika vyuo vikuu na taasisi ya elimu za juu, kwa sababu unaweza ukawa na kigezo cha kukopa kumbe kule katika taasisi ya chuo kikuu haujapata sifa za udahili. Kwa hiyo, waliokidhi wakawa 74,312. Kati ya hawa Bodi iliwapa mikopo wanafunzi 70,603.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utaona kwamba waliokosa hapa ni chini ya wanafunzi 3,000. Mwaka huu hali ikoje; mwaka wa fedha 2022/2023. Waliyoomba wanafunzi 97,760 baada ya uhakiki wa Bodi, waliostahili, wenye sifa za Bodi ni wanafunzi 85,876. Baada ya Bodi kufanya uhakiki kwa mujibu wa udahili, wanaostahili mwaka huu ni 80,502; lakini sasa mwaka huu bajeti wanayo kwa wanafunzi wa first year, kwa sababu tukumbuke Waheshimiwa Wabunge bajeti ambayo tulipitisha hapa ni bajeti ya shilingi bilioni 570 kama mwaka jana.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sababu mwaka jana waliongezeka sana, ina maana wanafunzi wanaoendelea, wale waliokuwa wanaendelea haiwezekani ukawatoa lazima uwapate. Kwa hiyo, kwa sababu bajeti ni ile ile, katika wanafunzi 80,502 wanaostahili kupata mikopo mwaka huu, kwa mujibu wa bajeti sio kwa mujibu wa sifa, ni 42,000. Sijui kama mnanipata hapo? Wanafunzi 80,000 wanaostahili au wenye sifa za kupata mikopo na ambao wamefanyiwa uhakiki, lakini bajeti ambayo tunayo ni ya wanafunzi 42,000 ndio ambayo tunayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, takriba wanafunzi 40,000 hawatapata mikopo, kwa hiyo ndiyo maana messages zimekuwa nyingi kwetu kuliko mwaka jana. Sasa, huu ndiyo msingi wa changamoto ambayo tunashughulika nayo, na ni muhimu kutibu tatizo badala ya kutibu dalili za tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri kwa taarifa ambayo Mheshimiwa Waziri alitupa; nadhani baadaye Serikali itapata nafasi ya kueleza kwamba wamewasiliana vizuri na Wizara ya Fedha na kuna maendeleo mazuri naamini kwa maelekezo yako Serikali itatoa maendeleo hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hiyo ndiyo changamoto, lakini habari njema ni kwamba…

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Kitila Mkumbo, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante, nilitaka kuongeza mnofu kidogo kwa Mheshimiwa Kitila kwamba lipo tatizo lingine ambalo linafanana na hilo. Kwamba mwanafunzi wa maskini ambaye hana uwezo wa kupeleka karo, amepewa sifa za kupewa mkopo na Bodi ya Mikopo lakini kigezo lazima afanye registration, ajisajili kwanza kwenye shule aliyopata ndipo wampe mkopo. Sasa kama hana hela ya kwenda kujisajili, maana yake chuo hakimtambui kama ana pesa za mkopo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kigezo nacho kitambulike kwamba kama kuna mwanafunzi maskini ana sifa za kupata mkopo na hana uwezo wa kujisajili, chuo kitambue kwamba mkopo wake wa asilimia mia kama amepewa, basi chuo kikubali apokee hiyo hela. Hela zikija ili aweze kujisajili, lakini wanamzuia, hawawezi kumpa mpaka ajisajili na hela hana. (Makofi)

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa muongozo huo mzuri na nitazingatia katika mchango wangu kwa dakika ambazo zimebaki. Tuliona sisi kama Kamati tukitoka hapa bila kugusia msingi wa tatizo, tutakuwa hatujatenda haki, lakini nashukuru kwa maelekezo yako.

Mheshimiwa Spika, sasa nichangie hilo la kwanza la mawasiliano. Mheshimiwa Waziri kwa maelezo yake na maelezo ya Bodi, alienda kwenye Bodi tarehe 12 Julai akatoa maelekezo na akaitambulisha Kamati ile ambayo ilikuwa ifanye kazi na Bodi wakaipokea.

Mheshimiwa Spika, katika hali ya kawaida, katika utendaji wa Kiserikali, Waziri alishamaliza kazi yake. Ina maanisha kwamba baada ya hapo vyombo vingine vilivyofuata vilitakiwa vifuatilie. Kwa mfano, Waheshimiwa Mawaziri wanafahamu kwamba Katibu wake wa Mheshimiwa Waziri angemwandikia Katibu Mkuu, kwamba alipokuwa kwenye ziara tarehe hii na Mheshimiwa Waziri ametoa maelekezo, moja, mbili, tatu, naomba kuwasilisha kwa utekelezaji, hilo halikufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Bodi wamekuja kupokea maelekezo rasmi ya Wizara tarehe 31 Agosti. Na kwa kweli kwa ushahidi ya maelezo ya Bodi na nyaraka ambazo waliwasilisha, mara walipopokea maelekezo ya tarehe 31 Agosti walitekeleza lile agizo kwa kasi ambayo hata sisi Wajumbe ilitushangaza. Hata hiyo kazi haijaanza, basi Mwenyekiti wa Kamati ameandika barua Wizarani akieleza kwamba, sasa nimepokea na tupo tayari kuanza kazi tarehe 31 Oktoba, ambayo ni juzi. Bodi baada ya kupata kibali cha Wizara, mara moja walishalipa na hela ya advance ya Kamati kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo katika mazingira hayo, utakuta kwamba Kamati ilipata ugumu from documentary evidence kwamba ni lini uweze kuihukumu Bodi kwamba imekwamisha maelekezo ya Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, kuna changamoto hiyo ya mawasiliano ambayo tumeieleza na tumetoa mapendekezo ambayo tumeyatoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba nami nichangie kwenye mpango huu, niongeze mambo matatu ambayo siyaoni kwenye mpango. Kabla sijaongeza hiyo, niseme kwamba mpango huu ni muhimu sana kwa sababu ndiyo mpango wa kwanza tangu tutoke kwenye janga la COVID- 19, lakini ndiyo mpango ambao utatuambia ni kwa kiasi gani tunaenda kukamilisha au ku-achieve our National Development Vision 2025. Umuhimu wake ni mkubwa sana na tunafahamu kwamba moja ya mafanikio ya jumla ambayo tuliyapata mwaka 2021 ni Benki ya Dunia kuitangaza Tanzania kwamba imefika uchumi wa kati (Lower Middle-Income Country) pamoja na kwamba suala hili itakuwa ni muhimu Mheshimiwa Waziri akalitolea msimamo baadae kwa sababu tunasikia takwimu zingine zinasema tumeshuka, nyingine tuko pale pale, ni muhimu Serikali ikaliweka vizuri jambo hili ni kubwa sana siyo jambo la kupita hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nilikuwa nasoma taarifa za World Bank kwenye website yao na Waheshimiwa Wabunge, mnaweza mka-google, wana-update kila baada ya muda fulani. Kwa mujibu wa takwimu hizi za Benki ya Dunia, nchi yetu mwaka 2021 ilikadiriwa kuwa na pato la dola za Marekani bilioni 67.78 na siyo bilioni 62. Ukifanya hesabu kwa idadi ya watu wa sasa hiyo inatupa GDP per capita income ya dola za Kimarekani 1,135.5. Kwa hivyo, utaona kwamba tumepanda kidogo kuliko mwaka 2020. Kwa hiyo, ni hoja kwamba tumeshuka haiwezi kuwa kweli na ni muhimu tukalinda mafanikio yetu kwa wivu mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ningeomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha utakapohitimisha hili jambo alitolee kauli nzito ya kueleweka ili nchi isibabaike. Tumeshuka au tuko pale?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo matatu ambayo ningependa kuyaangalia ambayo siyaoni kwenye mpango vizuri. La kwanza ni suala la umuhimu wa kuendelea kupambana na umaskini. Ukichukua mpango wetu wa maendeleo ukurasa wa kwanza kabisa kuna ujumbe mahususi wa Mheshimiwa Rais pale. Na katika ujumbe mahususi huo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan alieleza kwa uzito changamoto ya umaskini, na alitumia maneno haya naomba ninukuu; “Tunapoanza utekelezaji wa mpango wa tatu sote tunatambua changamoto nzito mbele yetu, umaskini bado unaendelea kuwepo nchini licha ya jitihada kubwa, zinazowekwa katika kuimarisha maendeleo ya watu. Aidha utofauti wa kiwango cha kipato na matumizi unaendelea kuwepo katika jamii zetu, ikiwa ni moja ya kati ya viashiria vikubwa katika kufikia malengo kusudiwa ya Dira ya Taifa ya Maendeleo. Moja ya sababu za msingi za maendeleo hafifu wa upunguaji wa umaskini licha ya ukuaji imara wa uchumi ni kutokufanikiwa kikamilifu kwa Tanzania katika kuongeza tija na uzalishaji katika sekta za msingi”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ndio maneno ya Mheshimiwa Rais kwenye utangulizi wa Mpango wa Maendeleo. Anatambua kwamba, bila kuwekeza katika sera za msingi za kuongeza tija hatuwezi kutoka. Kwa hiyo hilo ni jambo kubwa lakini ikifika Mpango wetu wa Maendeleo wa Miaka Mitano, lengo namba 12 linazungumzia umaskini tu; na linasema, kuongeza kasi ya ukuaji wa uchumi jumuishi na shirikishi kupitia mikakati ya kupunguza umaskini. Hili ni jambo la msingi sana katika mpango wetu wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti utafiti wa Benki ya Dunia unaonesha waziwazi kwamba kutokana na janga la Covid watu 140,000 katika nchi hii walipoteza kazi katika sekta rasmi. Watu milioni 2.2 walipoteza kipato. Utafiti unaonesha vilevile kwamba bila kuchukua hatua mahususi watu 600,000 watatupwa kwenye dimbwi la umaskini. Kwa hiyo ni muhimu mpango wa maendeleo uoneshe jitihada za kushughulikia umaskini bayana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesoma mpango katika kurasa 161 nilikuwa na-set pale, katika mpango mzima neno umaskini limejitokeza mara moja tu, na limetajwa kwenye suala la kushughulikia kunusuru kaya maskini. Hii haitoshi, tuwaombe wataalam wetu warudi katika mapendekezo ya mpango watuletee mikakati ya kupunguza umaskini katika nchi hii, hili ni jambo la msingi sana. Katika mpango tutakaokuja kuupitisha mwezi wa pili tuone bayana mikakati inayoshughulikia umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo sijaliona ni suala la idadi ya watu. Nchi yetu sasa tunafahamu hatubahatishi tena, tupo milioni 61.7 na tumekua kwa kiwango cha asilimia 3.2, ongezeko kubwa kuliko miaka yote ya sensa. 1989 mpaka mwaka 2002 ilikuwa asilimia 2.9, 2012 ilikuwa asilimia 2.7 sasa hivi ni asilimia 3.2 ndiyo kubwa kuliko tangu tuanze kuchukua sensa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ongezeko kubwa la idadi ya watu lina sura mbili. Sura ya kwanza ni fursa, kwamba mpo wengi kwa hivyo nyie ni soko. Sura ya pili ni kwamba mna uhakika wa wafanyakazi wenye nguvu za kufanya kazi kwa sababu mko wengi. Pia uzuri ni kwamba kwa structure ya population yetu asilimia 70 wapo chini ya miaka 35. Kwa hiyo kwa kweli watu wetu wengi tulionao katika nchi hii ni watoto na vijana. Na ndiyo maana hata mimi mwenyewe mwenye miaka 50+ siku hizi vijana wananiita mzee. Mzee kwa sababu gani? nimekuja kugundua hata kama watu wengi ni watoto na vijana wewe miaka 50+ wewe ni mzee bwana, kwa hili ni sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili uipate hiyo unahitaji nini? population dividends wanaita wataalam. Kwanza lazima uwekeze katika elimu sana. Lazima uwekeze katika mpango kupunguza umaskini, lazima uwe na chakula cha kutosha. Bahati mbaya sisi kwa sasa takriban kila kitu hakitoshi. Katika shule kama ni madarasa, kama ni waalimu, everything you talk about haitoshi, maana yake nini? lazima turudi katika miaka ya 1970, 1980, tuanze kuzungumzia suala la uzazi wa mpango, hili jambo haliwezi kukwepeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ilikuwa champion wa family planning 1970’s, 1980’s na ndiyo maana tukaweza kupunguza ongezeko la kasi kiasi hicho. Hapa tulipofika lazima hilo lifanyike, na mimi napendekeza kabisa kwamba tufanyie mabadiliko Tanzania Commission for Aids tuiongezee jukumu la family planning. Haya ni pendekezo langu ambalo nimeona kwamba ni muhimu kwamba ni muhimu yaingie kwenye mpango wetu wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho, tumesema kwenye lengo namba 11 kuimarisha jukumu la Mamlaka ya Serikali za Mitaa katika kuleta maendeleo na kuongeza kipato katika ngazi ya jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye mpango huu, huoni chochote kuhusu kuimarisha Local Government Authorities. Nimeshasema na ninarudia tena. Itakuwa ni vigumu sana kwa nchi hii kudhani kwamba tunaweza kupinga kasi ya maendeleo from the center. Nchi hii ni kubwa, ina watu wengi lazima tuimarishe Serikali za Mitaa. Na katika kuimarisha Serikali za Mitaa tunazungumzia income, vyanzo vya mapato katika Local Government Authorities havipo. Tungetaka kuona mpango wa maendeleo deliberately kabisa unaanzisha vyanzo vipya vya mapato…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Mkumbo kengele ya pili ahsante…

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii; na mimi nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake nzuri na hasa matumizi ya tafiti kwenye hotuba yake, amerejea tafiti mbalimbali; kwa kweli ni hotuba ambayo imenifurahisha sana. La pili; mipango yote ambayo Mheshimiwa Waziri ameeleza ili iweze kutekelezwa kikamilifu itahitaji fedha; na moja ya chanzo cha fedha kikubwa katika nchi hii ni utalii. Ni kwasababu hiyo na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge wengine kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa ubunifu wake wa kuja na The Royal Tour ambayo baadhi ya wataalam wa utalii wametuambia kwamba ina nafasi ya kuongeza volume utalii katika nchi hii mara mbili au mara tatu. Hiyo itatuongezea uwezo wetu wa kuweza kujitegemea lakini hasa ku-finance mambo haya mengi ambayo Mheshimiwa Waziri wa Nchi ameeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie maeneo mawili. Kwanza ni suala la hali ya utumishi wa umma nchini. Na niungane na nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge aliyemaliza kuongea kwa hotuba yake na mchango wake mzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utumishi wa umma ndiyo injini ya utekelezaji wa sera na sheria ambazo tunazitunga humu Bungeni, ndiyo injini ya utekelezaji wa Mpango wa Maendeleo wa Taifa, kwa hivyo lazima tuwaheshimu na kuwapa recognition ya kutosha watumishi wa umma. Na kuna kipindi kwakweli tunajisahau, tunajimwagia sifa sisi wenyewe wanasiasa tunasahau kwamba nyuma ya sisi kuna watumishi wa umma ambao wanafanya kazi kubwa ya wakati mwingine katika mazingira magumu. Mimi nichukue nafasi hii kuwapongeza sana watumishi wa umma wa nchi hii kwa kazi kubwa wanayoifanya katika kuendesha nchi yetu na Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utumishi wa umma kama alivyoeleza Mheshimiwa Waziri una changamoto nyingi; lakini nataka niongelee changamoto moja kubwa ambayo tushirikiane namna ya kuitatua. Ni kuhusu suala la uhaba wa watumishi wa umma katika sekta mbalimbali. Wakati mwingine tukilizungumza tunaliweka katika kiwango pengine hakiakisi uhalisia. Hebu tuangalie, nitoe mifano katika sekta saba kama muda utaniruhusu.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni elimu. Kwa mujibu wa taarifa za Serikali ambazo nimezichambua kupitia bajeti hii, Walimu wa Sekondari na shule za Msingi mahitaji ya nchi hii ni 433,992, Walimu waliopo ni 258,291, upungufu ni Walimu 175,701 sawa na asilimia 40.

Mheshimiwa Spika, sekta ya afya. Tunahitaji 208,232, waliopo 98,987, upungufu 109,295 sawa na asilimia 52.5. Lakini ukitaka kuangalia tatizo kubwa zaidi nenda kwenye zahanati na vituo vya afya kwa sababu huko ndiko zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wanatibiwa kwenye zahanati na vituo vya afya. Vituo vya afya na zahanati nchi hii vinahitaji watumishi 131,547, waliopo ni 48,579, upungufu 82,968 na asilimia 63.1 ni upungufu.

Mheshimiwa Spika, katika sekta ya maji afadhali kidogo ndiyo bora, watumishi 10,279 ndiyo mahitaji, Watumishi waliopo ni 9,207, upungufu ni 169 sawa na asilimia Moja tu ya upungufu. Kwa hiyo sekta ya maji tupo vizuri kwa kiasi cha kutosha. Kilimo (productive Sector). Tunazungumzia mahitaji ya Maafisa Ugani 20,000 waliopo ni 9,600, upungufu ni 13,400, sawa na asilimia 67 ya upungufu.

Mheshimiwa Spika, jumla kwa sekta hizi chache ambazo nimezitaja tunazungumzia tunahitaji Watumishi wa Umma 1,238,089, waliopo 679,955, upungufu ni 558,134 jumla ya upungufu ni asilimia 45 maana yake nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais ameeleza vizuri hapa kwamba Serikali mwaka huu itakwenda kuajiri na tumepata kibali cha staff 30,000 na tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutoa kibali hicho. Lakini tunazungumzia 30,000 kati ya upungufu wa 679,955, maana yake tunakwenda kutatua tatizo kwa kiwango cha asilimia 4.4. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimefanya hesabu, trend ikiwa ni hii ili tuweze kutatua gap hii tutahitaji miaka 21, ili ku-address hii gap iliyopo we need 21 years. Ni wazi kwa saizi ya uchumi wetu ni wazi kabisa haitawezekana ku-address tatizo hilo kwa kutoa tu vibali. Ukisoma taarifa za Wizara mbalimbali wanaeleza changamoto ya ajira solution yake nini? Tumeomba kibali utumishi, yaani ndiyo solution inaishia hapo. (Makoni)

Mheshimiwa Spika, sasa nataka kutoa mapendekezo nikiamini kwamba kwa kweli hata iwe ni Serikali ya Marekani kwamba inaweza ikaajiri watumishi hawa tukaziba hii gap haitawezekana. We need to think of alternative ways na Mheshimiwa Waziri utusaidie, mje na mikakati mipya namna ya kutatua tatizo hili. Naomba nitoe mapendekezo manne.

Mheshimiwa Spika, moja, kwanza ifanyike National Audit ya Watumishi wa Umma. Nilipokuwa Katibu Mkuu Wizara ya Maji tuliamua kufanya National Audit ya Watumishi wa Umma tukaenda tukagundua kwamba kuna kazi zinafanywa na wafanyakazi wawili kwa kazi moja, ndiyo ikatusaidia ile ndiyo unaona upungufu katika Wizara ya Maji ni asilimia moja kwa sababu ya National Audit ambayo tulifanya. Serikali ifanye National Audit tupate mahitaji halisi ya Watumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, tutekeleze sera ya D by D kwa uhakika. Kwa mfano, kwa nini Serikari iajiri Maafisa Ugani? Kwa nini mapato ya mazao ya kilimo katika kijiji yabaki hapo wakaajiri wao, kwa nini tusitumie mtindo huo? Hiyo inaweza ikaangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nadhani la mwisho tuweke mazingira mazuri kwenye sekta binafsi ili kwamba kwa mfano katika shule, asilimia Tatu peke yake ya shule ndiyo za sekta binafsi kwa shule za msingi zilizobaki ni za Serikali. Tukiweka mazingira mazuri watu binafsi wafungue shule nyingi zaidi za msingi wataajiri Walimu, hivyo hivyo katika sekta ya kilimo na zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho ni Sekta ya Madaktari. Madaktari wengi katika hospitali za binafsi wanatoka sekta ya umma, ni muhimu tuweke mazingira mazuri ili sekta ya umma ya afya iweze kuajiri watumishi wake badala ya kutumia watumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimalizie mchango wangu na eneo moja muhimu la haraka. Suala la bodaboda, machinga lipo katika ukurasa wa 42 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri, tuelewe vizuri structure ya uchumi wetu ikoje, niwapeni mfano katika Jimbo la Ubungo sisi tunazo Kata Nane, Jimbo la Ubungo tuna bodaboda 4,891. Kimara 728, Mabibo 683, Makuburi 847, Makurumila 839, 655, 656,645 na Ubungo 838. Kata ya Ubungo yenye bodaboda 838, bodaboda wanne wana Masters, bodaboda 21 ni Graduate, Digrii ya Kwanza, hiyo ipo katika Dar es Salaam huko wengi ni Form Four, Form Six, Graduate, kwa hivyo hii ni sekta muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wakuu wa Mikoa waelezwe na Mheshimiwa Waziri mtupe mtamko hapa, hii tabia ya kutoa matamko yakusumbua sekta binafsi yaishe. Tungetaka tamko hapa la Waziri atueleze kwamba anapiga marufuku bodaboda kupigwa marufuku kuingia Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi ina vipaumbe Sita, kipaumbele cha Sita kinazungumzia kuajiri wafanyakazi Milioni Nane kutoka sekta iliyorasmi na isiyorasmi tutapataje Milioni Nane tukianza kuwasumbua watu hawa? Hawa ndiyo ajira zetu hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuliahidi Dar es Salaam kwamba, tulitoa ahadi kwa bodaboda hamtapigwa marufuku tena kwenda katikati ya Jiji, sasa tupate tamko la Serikali kwamba hili tamko la jana ni la mwisho kusumbua bodaboda katika nchi hii, hawa ndiyo wenye uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na Mwenyekiti wangu wa Kamati Mheshimiwa Nyongo kwa kupongeza Mheshimiwa Waziri na timu yake yote akiwepo Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya. Niwapongeze sana kwa maboresho ambayo yanaendelea kuboresha sera pamoja na mitaala yetu, tunawatakia kila la kheri na sisi tutawapa ushirikiano wote kama Kamati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatekeleza dira ya maendeleo na Mpango wetu wa Tatu wa Maendeleo, nyenzo kubwa ya kutekeleza hayo ni uwekezaji katika rasilimali watu. Nyenzo kubwa ya kujenga rasilimali ni elimu na nyenzo kubwa ya kutoa elimu ni Walimu. Mchango wangu leo ni kuhusu Walimu na hasa kwenye kuchangia kwenye maboresho ambayo yanaendelea katika taaluma ya ualimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Profesa Issa Shivji aliwahi kusema, mmoja wa maprofesa maarufu hapa Profesa wa kisomo, ukitaka Taifa bora boresha elimu, ukitaka kuboresha elimu boresha Walimu, ukitaka Taifa la watu wanaojiheshimu heshimu Walimu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mwalimu Nyerere aliwahi kusema na namnukuu pia, alisema kwa Kiingereza: “No education policy however good can succeed, without well trained professional carder.” (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo maboresho ambayo tunayafanya haya ya kisera na kimitaala, yatafanikiwa sana kama yakienda sambamba na uwekezaji katika taalum ya ualimu na Walimu wenyewe. Kada ya ualimu Tanzania ina changamoto nyingi lakini naomba nizitaje tatu tu na nitoe mapendekezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tumeshasema na Mheshimiwa Mwenyekiti wangu amesema tuna changamoto ya uhaba wa Walimu tulishalisema hapa, tuna upungufu sasa hivi 175,000 takriban 40% lakini changamoto kubwa zaidi ni kwa upande wa Walimu wa sayansi. Kwa sasa kwa mfano tunahitaji Walimu wa sayansi na hesabu 70,327, waliopo ni 23,647, unazungumzia upungufu wa 66%, takriban theluthi mbili, huwezi kujenga uchumi wa viwanda bila sayansi, hesabu na teknolojia. Kwa hiyo, ni lazima tuwekeze katika ku-train Walimu wa hesabu, sayansi na teknolojia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2026 tutakapomaliza kutekeleza mpango wetu wa maendeleo ambao tunao, inakadiriwa kwamba tutakuwa na wanafunzi wa elimu ya awali msingi na sekondari 23,600,000. Hawa tutahitaji Walimu 724,000, maana yake changamoto ni kubwa. Kwa hivyo tunazungumzia ili tuweze ku-cover hizi changamoto tufikie hayo malengo ambayo tumejiwekea, tunahitaji kuajiri Walimu kila mwaka takriban Walimu 100,000. Sasa hivi tunaajiri Walimu 10,000 hiyo itachukua miaka zaidi ya 18 kuweza kuziba pengo. Sasa hiyo ni changamoto ambayo lazima tuione.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya pili kwa upande wa Walimu ni kwamba, Mwalimu ana mabosi wengi mno. Moja Mwalimu anaajiriwa na Mkurugenzi wa Halmashauri, anapandishwa cheo na Tume ya Utumishi ya Walimu, Mwalimu akiwa na shida ya mshahara wake inabidi aende kwa Katibu Mkuu Utumishi, Mwalimu akiwa na changamoto na mitaala inabidi aende Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Juzi mwaka 2018 tukaunda Bodi ya Walimu inaitwa Tanzania Teachers Professional Board ambayo ipo upande wa Wizara ya Elimu maana yake na yenyewe inakwenda kumbebesha Mwalimu mzigo.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya tatu kwa leo ni ukweli kwamba ambayo wote tunajua ni maslahi duni kwa Walimu wetu na kukosekana kwa motisha. Nataka nitumie muda uliobaki nitoe mapendekezo saba kwa ajili ya kuboresha na kutatua hizi changamoto ninazozizungumza. Mapendekezo saba ambayo yataingia Mheshimiwa Waziri akiyapenda aingize katika mchakato wake wa maboresho. Changamoto ya kwanza kuhusu kupunguza upungufu wa Walimu napenda kutoa mapendekezo manne ambayo yatatusaidia kupata Walimu 44,000 kwa kila mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, hakuna shaka kwamba Serikali pekee yake kwa ukubwa wa changamoto ya Walimu kwa maana ya idadi haitaweza kuijibu hii changamoto, kwa sababu tunazungumzia kuajiri Walimu 100,000 kila mwaka, maana yake Serikali iache shughuli zingine zote ishughulike Walimu tu, hicho hakitawezekana. Napendekeza Serikali tuweke mazingira mazuri ya kuvutia sekta binafsi kuwekeza katika elimu kwa sasa kwa mfano katika elimu ya msingi tupo chini ya 10% ya shule ambazo zinamilikiwa na private sector, kwa nini? Kwa sababu nyingi lakini mojawapo ni kwamba tuna kodi 13 katika shule. Ukianzisha shule hapa, utalipa kodi 13 haya mazingira yanafanya ada ziwe kubwa, mazingira yanafanya watu washindwe kufungua shule.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wetu wa halmashauri waelekezwe kwamba wewe kufungua shule hapa City Council Dodoma, mtu akifungua shule yake wanafunzi wanaokwenda pale, inamsaidia Mkurugenzi wa Halmashauri kwa sababu wale wanafunzi, vinginevyo angewabeba yeye, lakini Wakurugenzi wetu wanakimbilia sana ile service levy, kwa hiyo tuweke mazingira hayo. Tukifanya hivyo tunakadiria kwamba tuna uwezo wa kuongeza Walimu mpaka tukapata Walimu 5,000 kutoka private sector.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la pili, Serikali iweke malengo ya kuajiri Walimu 20,000 mpaka 30,000. Tukiwaajiri Walimu 20,000 inaweza ikasaidia kuliko kuajiri walimu 10,000. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la tatu, muda wa mafunzo ya ualimu katika Vyuo Vikuu uongezwe, uwe miaka minne na ule mwaka wa nne wote utumike kwenye mafunzo mashuleni. Kwa hiyo tutapata Walimu kati Walimu 15,000 mpaka Walimu 20,000 kila mwaka kutoka katika vyuo vikuu na hawa hatuwalipi wanaendelea kulipwa na Bodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la mwisho hapa, tupunguze nafasi ya utawala katika elimu, tufute kada ya Maafisa Elimu Kata, tuimarishe menejimenti ya shule ili watu hawa waende kufundisha. Tunazungumzia kupata Walimu 3,956, hakuna sababu ya kuwa na Maafisa Elimu wa Kata, hakuna sababu kama tuna uongozi imara wa shule, kwa nini tuwe na Afisa Elimu wa Kata, kwa hiyo tuondoe hiyo watu wakafundishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo la mwisho kwenye upande wa motisha, sasa niingie kwenye motisha kwa sababu ya muda ni suala la motisha kwa Walimu. Naomba kwa heshima na taadhima turudishe posho ya kufundisha kwa Walimu (teaching allowance). Tunazungumzia kitu kidogo, tunazungumzia Sh.4000 kwa siku kwa Mwalimu, maana yake kwa siku tano Sh.20,000 kwa mwezi Sh.100,000. Hii itahamasisha Walimu, ilikuwa ni vitu muhimu sana, walimu wameshaomba mara nyingi, Waziri wa Fedha yupo hapa, hatuwezi kushindwa kuweka Sh.100,000 kwa Mwalimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, tunaomba Teachers Service Commission…

NAIBU SPIKA: Waziri wa Fedha nimesikia taarifa au siyo wewe? Siyo wewe au basi endelea.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Naomba Teachers Service Commission ipewe nafasi ya kufanya kazi kikamilifu. Kwa kufanya hivyo, hatuna sababu ya kuwa na Teachers Professional Board kwa sababu majukumu yake mengi yapo ndani ya Teachers Service Commission.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie mchango wangu kwa shukran za pekee kwa hili ambalo limefanyika hapa watu wengi wanalichukulia ni mafuta tu, lakini kitendo cha Mheshimiwa Rais cha kusikiliza maoni ya Bunge, akaheshimu badala ya kutangaza mwenyewe jana akaamua kuleta hapa, ni kiwango cha juu cha kuheshimu utawala bora. Ameliheshimisha Bunge na sisi Wabunge tuna wajibu wa kumheshimiwa Mheshimiwa Rais. Tunampongeza kwa hatua hii, tutaendelea kumuheshimisha, tutaendelea kutoa maoni ya kujenga ili Serikali yetu iende vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika na mimi nashukuru kwa kunipa nafasi na nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa Mbunge wa Biharamulo Magharibi kwa kuleta hoja hii. Mambo matatu tu katika kuunga mkono hoja hii. Jambo la kwanza ni kihistoria kidogo.

Mheshimiwa Spika, siku ya tarehe 4 Julai, 2001, nchi yetu ilikumbwa na msiba mkubwa. Tuliondokewa na Makamu wa Rais Mheshimiwa Dkt. Omar Ali Juma; na Mheshimiwa Benjamini William Mkapa, Mungu amrehemu, wakati analihutubia Taifa alitumia nafasi hiyo kwa kutumia maisha ya Dkt. Omar Ali Juma kutoa mafunzo ambayo tumeyapata. Kwamba tuna mafunzo sita kuhusu sifa za msingi ambazo kiongozi wa kitaifa Tanzania anapaswa kuwa nazo, alitoa sifa sita. Na mimi miaka miwili ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ninaridhika kwamba hizi sifa ambazo Mheshimiwa Benjamini William Mkapa alizitoa tarehe 4 Julai, 2001 Mheshimiwa Rais anazo; na kwa ridhaa yako naomba nizitaje.

Mheshimiwa Spika, sifa ya kwanza ni utu na uadilifu, sifa ya pili aliitaja upendo na heshima kwa watu wote, sifa ya tatu kupenda kazi na kutumikia wananchi badala ya kupenda kutumikiwa na kutukuzwa, sifa ya nne aliitaja kuweka mbele maslahi ya Taifa na Watanzania badala ya maslahi binafsi au ya kikundi, sifa ya tano unyenyekevu badala ya kupenda makuu na sifa ya sita, na kwa maoni yangu ni muhimu sana, kuzingatia kikamilifu misingi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, na aliitaja misingi hii tisa ambayo kwa hakika Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan anaizingatia kikamilifu. Msingi wa kwanza wa Taifa utu, pili haki, tatu usawa, nne fursa sawa, tano amani, sita umoja, saba upendo, nane mshikamano na ya mwisho namba tisa ambayo ni muhimu sana Muungano wetu wa Tanzania Bara na Zanzibar. Hakuna shaka katika miaka yetu yote katika nchi hii Muungano wetu upo salama sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili,hakuna shaka kwamba mambo haya yote Mheshimiwa Rais anayafanya kwa utashi kwa ujasiri na kwa kuzingiatia katiba na Sheria za nchi yetu. Lakini kumekuwepo na jitihada za hapa na pale kwa baadhi ya watu kujaribu kumtenganisha Rais wetu na Chama cha Mapinduzi. Nataka nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa sababu anayoyafanya haya yote ili kutekeleza kikamilifu Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Spika, na nitoe mfano, katika Ilani yetu paragraph118 ukurasa wa 166 tumesema hivi; katika kipindi cha miaka mitano ijayo, Chama cha Mapinduzi kitaendelea, sikiliza hiyo, kuheshimu na kulinda misingi ya demokrasia na haki za binadamu kwa ajili ya ustawi wa Taifa hili. Kwa hiyo suala hili Mheshimiwa analifanya kwa kutekeleza Ilani ya CCM kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, lakini paragraph ya 250 ukurasa wa 298 ameweka wazi. Ilani inasema katika kipindi cha miaka mitano ijayo Chama cha Mapinduzi kitaendelea kutekeleza jukumu la kihistoria la kimapinduzi la kuongoza pambano la kutetea na kulinda utu, usawa na haki chini ya misingi ya Ujamaa na Kujitegemea. Katika kutimiza wajibu huu CCM itaendelea kusimamia mambo matano yafuatayo, jambo la nne ni kuimarisha demokrasia nchini. Kwa hiyo wale wanaodhani kwamba wanajaribu kumtenga Rais na CCM wamenoa ni sehemu Rais anatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho; baada ya kupokea report ya CAG juzi, Mheshimiwa Rais ameshatekeleza jukumu lake, yamebaki majukumu mawili. Jukumu la kwanza kwa Bunge hili na jukumu la pili ni kwa Serikali kupitia Mawaziri wetu. Mimi niwaombe katika muda tulionao siku 88 za kukaa hapa Bungeni tunatarajia kuona kutoka Serikalini majibu yatakayo jibu zile changamoto za kimfumo, kisheria na kikanuni; tuzione kutoka kwa Mawaziri.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wetu Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Rais kaongea kwa uchungu sana kama alivyotoka kusema Mheshimiwa Ole-Sendeka kazi yetu; hiyo ni kazi ya Serikali, kwa upande wetu sisi. Sisi Tanzania hatuna utamaduni wa kupisha. Kazi yetu Wabunge tuwaoneshe wenzetu, ambao Mheshimiwa Rais amewasema, mlango wa kutokea. Kazi hiyo duniani huwa haifanywi na Serikali, huwa inafanywa na Bunge. Tunatarajia Bunge hili, watu wote ambao Mheshimiwa Rais amesema wapishe hawajaona mlango sisi tuwaoneshe mlango. Katka miezi hii mitatu hilo ni jukumu la msingi la Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,baada ya kusema hayo na mimi nichukue nafasi hii kwa heshima kubwa ninaunga mkono hoja hii tuendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Rais na Rais popote alipo atembee kifua mbele ajue Bunge hili linamuunga mkono, lipo naye usiku na mchana. Ahsante sana. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (No. 3) Bill, 2023
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MIPANGO NA UWEKEZAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja. Naomba nitoe ufafanuzi wa jambo moja tu kuhusu composition ya Bodi ya EPZA kwa nini Katibu Mkuu asiwepo.

Kwanza dhana ya wale Makatibu Wakuu wawili kuwepo ni kwa sababu Bodi ya EPZA pamoja na mambo mengine inafanya uamuzi wa uwekezaji katika eneo husika. Kwa hiyo, tukishafanya uamuzi wa kujenga industrial park, kazi ya Serikali kubwa ni kuwezesha ujenzi wa miundombinu husika; kama nishati, maji, barabara na kadhalika. Ilionekana kwamba wawepo ili uamuzi ukishafanyika, wahusika wa miundombinu ile wawe tayari ni sehemu ya uamuzi ili waweze kuharakisha utekelezaji wake. Kwa hiyo, ndio ni sababu ya msingi kwa nini wale Makatibu Wakuu wawili unaona wapo pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa nini Katibu Mkuu husika hayupo ni kwa sababu Waziri wa Sekta husika ndio Mwenyekiti, kwa hivyo kawaida unapomwona Waziri kimsingi unamwona Katibu Mkuu kwa sababu anayemwandaa Waziri ni Katibu Mkuu. Kwa hiyo kimsingi Katibu Mkuu wa Sekta husika yupo na kawaida huwa anahudhuria vikao. Sio mjumbe lakini Katibu Mkuu huwa anahudhuria kama Ex- Officio. Kwa hiyo, nadhani hilo halina ugumu na kama alivyosema Mheshimiwa Olelekaita, Mtendaji Mkuu wa EPZA kimsingi anafanya kazi chini ya usimamizi wa Katibu Mkuu. Kwa hivyo kimsingi Katibu Mkuu yupo pamoja na kwamba haonekani kwenye orodha ya Wajumbe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nilitaka nitoe ufafanuzi huo mdogo katika kuboresha hoja hii. Nakushuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwanza nianze kwa kutangaza maslahi kwenye Wizara hii siyo maslahi yale ya kikanuni maslahi ya kifedha ni ukweli kwamba nilipata bahati ya kutumikia Wizara hii kama Katibu Mkuu kwa miaka mitatu na nusu na kwa nafasi hiyo nilifanya kazi kwa karibu sana na Mheshimiwa Jumaa Aweso. Kwanza aitwi Juma anaitwa Jumaa Hamidu Aweso nilimpokea pale nataka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nithibitishe kwamba Waziri huyu ni mtu makini, ni mzalendo sana, ni mchapakazi, ni mnyenyekevu lakini muhimu sifa za ziada ambazo siyo lazima uziseme na kazi yake ni mcheshi, ni mchangamfu sana na watu waliyofanya kazi Wizara ya Maji wanafahamu kwamba anafahamu kiswahili vizuri ndiyo maana katika hotuba yake zimejaa methali za kiswahili jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Mamlaka ya Maji Jijini Dar es salaam DAWASA kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya Mkoa wa Dar es salaam, hususani Jimboni kwangu mimi nina kata 8, mitaa 46 zile 86 ambazo amezisema sisi tulishazivuka siku nyingi. Kwa hiyo, tuna bahati, tunashukuru kwa hilo. Lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri alikuja mtaa ulikuwa umebaki Mtaa wa Golani tulikwenda nae mpaka kule mlimani sana, wale wananchi wamenituma asubuhi hii nikushukuru sana wanapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru sana Engineer Edison Meneja wetu wa Ubungo na Engineer Julieth John Meneja wa Magomeni wanafanya kazi kubwa. Nichukue nafasi hii pia kumponeza mdogo wangu Cyprian Luhemeja kwa uteuzi ambao ameupata, amefanya kazi kubwa Dar es Salaam tunarajia kwamba atasaidia katika nchi na tumtakie Engineer Kiula na wengine wote waendelee kufanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninataka niombe Engineer Julieth tumeisha ongea, Engineer Lidya ile tumetengeneza mradi mzuri wa maji taka, Mtaa wa Manzese, National Housing na Sinza na sehemu zingine lakini mitaa ni critical kwa sababu ina shida kubwa sana ya maji taka tumeisha zungumza hili niwaombee mlitekeleze vizuri ili wananchi wetu waweze kukaa vizuri pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, sekta ya maji hakuna shaka, katika miaka ya hivi karibuni imepata mafanikio makubwa ambayo Mheshimiwa Waziri ameyaeleza. Nataka nitumie dakika ambazo zimebaki kueleza mafunzo ambayo tunayapata yanayotokana na mafanikio katika sekta ya maji na wale ambao wapo humu ndani muda mrefu wanafahamu ni nikiwa Katibu Mkuu tukija hapa Mwaka 2017 palikuwa hapakaliki. Tukikaa pale mlikuwa mnatupiga nyundo za kutisha, ukitoka hapo unamuomba waziri likizo ya wiki nzima baada ya bajeti kupita lakini hii kazi ilikuwa ni kubwa lakini baada ya muda mfupi kazi kubwa imefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mafunzo matano kama muda ukiruhusu moja; ni umuhimu wa kuwa na taasisi imara katika usimamizi wa shughuli za Serikali. Sekta ya maji inasimamiwa na taasisi kubwa tatu tunayo mabonde ya maji, mamlaka za maji ambazo zipo kwenye mijini na miji midogo na tuna RUWASA hii ambayo mmeipigia makofi mengi. Hizi ni Taasisi ambazo zinafanya kazi kubwa, kwa hiyo, nikusii Mheshimiwa Waziri uendelee kuzipa nguvu taasisi hizi kwa sababu kwakweli ndiyo miguu yako.

Mheshimiwa Naibu Spika, funzo la pili; ni umuhimu wa kuwa na mipango ya muda mrefu na kuishikilia. Sekta ya maji inaongozwa amesema Mheshimiwa Waziri na Program ya Maendeleo ya Sekta ya Maji water sector development program. Sekta hii imekuwepo kwa takribani miaka 20 na kila Waziri akija anakabidhiwa nyaraka hii na anatembea nayo, tofauti tu ni kasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekaa pale Mawaziri kadhaa alikuwepo Mheshimiwa Jumanne Maghembe, akaja Mzee wangu Kamwelwe akaja Profesa Mbarawa na wengine tofauti ni kwamba, wanatekeleza program hii hii hawabadilisha hata nukta. Tofauti kubwa ni kasi, kijana anakasi kubwa huyu, anakimbia zaidi, na kwa sababu yeye amevunja rekodi ya Jakaya Kikwete, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, amevunja rekodi, kwa sababu yeye ndiye mdogo kuliko wote sasa hivi katika Mawaziri wote wa Wizara ya Maji tangu Wizara hii iundwe. Alikuwa anashikilia rekodi Mheshimiwa Jakaya ameishapitwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, funzo la tatu; muhimu ni muhimu wa kuheshimu, kuwajali na kuwapenda watalamu wetu. Sekta ya maji ni moja ya sekta ambazo zina heshimu sana watalamu wake. Kwa hiyo, ni jambo muhimu tuwape nafasi, tuwaheshimu, kwa sababu ukweli ni kwamba mkono mmoja hauchinji ngo’mbe. Mheshimiwa Waziri, yuko hapa ana ng’ara lakini nyuma yake kuna vijana wakakamavu, waliyosoma vizuri, wanafanya kazi yeye anawapa nafasi. Hili ni jambo la msingi ambalo lazima aliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la nne; ni umuhimu wa uwekezaji. Sekta ya Maji inapata fedha kutoka mfuko wa maji jambo hili ni jambo zuri la kushukuru kwa kweli liendelee, kwa sababu hii ndiyo hasa nguzo ambayo inafanya miradi wa maji itekelezwa kwa ukubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tano; sekta ya maji na sekta za huduma zingine zinahitaji utulivu na tumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa kuipa sekta hii maji utulivu mkubwa sana kwa kiwango ambacho watalam wanafanya kazi yao kwa kutulia, kwa kutumia utaalam wake, sekta hizi ni ngumu. Katika hilo tatizo la sekta ya maji ni kwamba inapambana ni kama kila mara goli linapanuka kwa sababu leo anazungumzia asilimia 86
lakini kesho inaweza ikashuka kwa sababu ya ukuaji wa idadi ya watu hiyo ndiyo changamoto kubwa. Kwa hiyo, ni muhimu sana tuendelee kuwekeza fedha katika sekta hiii ili tuendelee kushughulikia miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la miwisho nichukue nafasi hii kuiba muda wako kama Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Elimu, Utamaduni na Michezo moja kuwapongeza vijana wetu wa yanga kwa mechi yao ya leo. Kwa sababu wamefanya kazi kubwa, wapo nusu fainali na la pili kuwatakia kila kheri katika mechi yao ya leo, leo ni siku kubwa katika… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Zungumzia hoja iliyoko mbele yako. (Vicheko)

MHE. PROF. KITILA M. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo najua hilo utakuwa umelizingatia hata wewe mwenyewe tunawapongeza vijana wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi. Naomba nianze kwa kutambua kazi kubwa ambayo wenzetu wanaifanya, na hasa nataka kutambua uamuzi wa Serikali na wa Rais wetu na Mheshimiwa Waziri wa kuweza kuwapitisha wenzetu wawili kwenda kugombea kwenye nafasi kubwa sana huko duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninazungumzia Mheshimiwa Spika wetu, Dkt. Tulia Ackson, anayegombea Urais wa IPU, na mimi naamini, ninamfahamu tangu chuo kikuu, ni mtu sahihi sana kwa nafasi hiyo. Kwa hiyo tuiambie dunia kwamba amepatikana mtu sahihi wa kuongoza chombo chetu hiki muhimu na wasitie shaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini imezungumzwa hapa kwamba Mheshimiwa Ambassador Liberata ni mtu mahiri, muhimu sana, na hiyo nafasi itakuwa imepata mtu sahihi. Kwa hiyo niishukuru sana Serikali kwa uamuzi sahihi sana wa kuwatanguliza hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni swali kwa kweli, kwamba kwenye zile hatua nne za Jumuiya yetu ya Afrika Mashariki, tulianza na customs union, tukaja soko la pamoja, lakini tarehe 31 Novemba, 2013, tukasaini protocol ya monetary union, ni miaka kumi, inaisha mwaka huu. Nataka kujua tupo hatua gani; na je, hatuoni haja ya kuharakisha mchakato huo tukizingatia kwamba sasa hivi tunazungumzia Dola ya Marekani ikienda kusambaratika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani mnafahamu, sasa hivi duniani, Middle East, hapa BRICS wanazungumzia kuanzisha fedha yao. Hatuoni ni muda sahihi sisi kuwa na fedha yetu Jumuiya ya Afrika Mashariki; East African Currency, hatuoni kama muda umefika? Ningeshukuru sana Mheshimiwa Waziri kama hili nalo ungeweza kulitolea ufafanuzi wakati una-wind up.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, nataka niongeze sauti kidogo, mimi sizungumzii uraia pacha kivile, na hili jambo lilizungumzwa vizuri sana kwenye hotuba ya Mwalimu Nyerere. Mara baada ya nchi yetu kupata uhuru na kuwa Jamhuri, tarehe 10, Desemba, kwenye Bunge letu, Mwalimu alitoa hotuba moja muhimu sana ambapo alieleza tunakwenda kujenga Taifa la namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na wakati huo kulikuwa na matabaka makubwa kati ya Wazungu, Wahindi, Waarabu na Waafrika. Na alijaribu kuwatia moyo, kwamba ninyi Wazungu hamjapoteza chochote kwa sababu bado uchumi upo mikononi mwenu, mna elimu zaidi; na Waafrika akawaambia mna political control, kwa hiyo tukiunganisha hizi forces mbili tunaweza kwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa kweli wakati huo kulikuwa na wasiwasi, suala la uraia lilikuwa kubwa, na Mwalimu alilizungumzia kwa kirefu sana. Lakini hoja ya msingi kwa upande wangu, suala kiuchumi ni zuri, lakini kwa kweli ni secondary, hoja ya msingi hapa tunalindaje haki za asili, haki za Kimungu? Kitila Mkumbo kuwa Mtanzania si chaguo lake, ni jambo la asili, jambo la Kimungu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna kati yetu hapa ambaye amechagua awe Mtanzania, au Mganda au Mkenya, uraia wa kwanza ni wa asili, unazaliwa kuwa raia wa nchi fulani. Mambo mengine ya kujitakia unaweza ukaamua uende kutafuta uraia wa nchi nyingine. Lakini kwa kweli jambo la msingi kuliko yote ni kwamba huyu mtu ambaye kwa Kimungu kabisa amezaliwa kuwa Mtanzania, na baadaye ameamua kwenda kusaka fursa, na kwa mujibu wa Katiba yetu Ibara ya 17(1) inasema hivi; 17.-(1)Kila raia wa Jamhuri ya Muungano anayo haki ya kwenda kokote katika Jamhuri ya Muungano na kuishi katika sehemu yoyote, kutoka nje ya nchi na kuingia, na pia haki ya kutoshurutishwa kuhama au kufukuzwa kutoka katika Jamhuri ya Muungano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi nimekaa hapa, mmenisomesha, nimeamua kwenda kutafuta kazi Afrika Kusini, nimepata. Lakini kule Afrika Kusini kuna hati fulani ili uzipate lazima uchukue mambo yao fulani; kitendo hicho kinaninyan’anya haki yangu ya Kimungu ya kuwa Mtanzania kwa sababu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ukisoma nchi nyingi ambazo zinapinga, hazitaki uraia pacha, zipo, hata Sweden. Lakini kitu kimoja ambacho wamekilinda ni haki ya uraia wa watu wao. Kwa hiyo wewe kachukue uraia wowote, lakini wewe ni Mtanzania, wewe ni Mswiden, wewe ni Mwingereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hakuna mtu anayezungumzia hapa kwamba eti atoke mtu kutoka nchi nyingine aje apewe Uraia wa Tanzania, hilo hatulipiganii, tunachopigania na kinachozungumzwa hapa; kwa nini turuhusu Mtanzania apoteze haki yake ya Kimungu kwa sababu tu amekwenda kutafuta fursa katika nchi nyingine? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na sasa hivi tunazungumzia, duniani, takwimu zinaonesha kabisa, moja ya njia za kutatua tatizo la graduate unemployment, tatizo la ajira ni kubwa, lakini tatizo kubwa la ajira kuliko yote ni tatizo la ajira ya watu ambao wamekwenda shule, wa vyuo vikuu hawa, hilo ndilo tatizo kubwa. Kwa hiyo njia ambayo zinafanya nchi nyingi ni kuwaandaa watu wao kuwa global citizens ili wakatafute kazi huko duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukisukuma hilo unaondoa vikwazo. Kwa hiyo hili jambo kama litakuja kwa uraia pacha, ama hadhi maalum, kwangu siyo hoja kubwa, hoja kubwa ni tunalindaje haki za watu wetu ambao ni Watanzania wanapokwenda kutafuta fursa kwenye nchi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hata kiuchumi, uchumi watu wengi wamesema hapa, vitu gani vinakwamisha watu wetu? Sisi watu wetu wengi wanakaa nje vizuri tu, ukiangalia idadi ya Watanzania, Waganda, Wakenya, hatutofautiani sana kwa walioko nje, lakini kwa nini remittance za wenzetu ni kubwa kuliko za kwetu? Kwa hiyo zimefanyika studies na zinaonesha, ya kwanza ni kwamba Mtanzania akiwa nje anakuwa hana confidence, kwa hiyo ni jambo ambalo lipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile hata watu wetu kutoka nje ni changamoto, inaonesha kwamba kwa East Africa Watanzania ndio watu ambao wanaongoza kwa kutokupenda kutoka nje, ambayo siyo faida kwa leo. Kwa leo ungetaka kuwa na watu ambao wanachangamkia fursa duniani na ndani ya nchi yao. Kwa hiyo nadhani hili ni jambo la msingi la kiliangalia, whatever form we are going to decide, kama ni uraia pacha, kama ni hadhi maalum, lakini ni jambo ambalo lazima tuliangalie kwa umakini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita nadhani Daily News wametoa taarifa, walikuwa wanamnukuu Mheshimiwa Rais, inaonesha kwamba ukiangalia hizo hela kutoka nje (remittance) na uwekezaji kutoka nje kwa Watanzania imefikia 2.5 trillion shillings; ni pesa nyingi. Kwa hivyo lazima Mheshimiwa Waziri uangalie ni namna gani utatengeneza mazingira mambo mawili yatokee; Watanzania wengi wachangamkie fursa za kiuchumi zilizopo duniani, lakini pia waliopo kule duniani wachangamkie fursa hapa nyumbani kwa maana ya uwekezaji. Hiyo lazima tuweke mazingira mazuri ya kufanya hivyo kwa sababu ni jambo la msingi. Kwa hiyo hili jambo likamilishwe mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonesha kabisa kwamba wameshazidisha, hela ambazo zinakuja kutoka kwa hawa zinazidi hela ambayo tunapata ya kahawa, cashewnuts, tumbaku na chai ukiunganisha. Hela za watu waliopo nje (diaspora), ni kubwa, kwa hiyo siyo jambo ambalo kwa kweli tunaweza kuendelea kuliangalia kwa jicho ambalo siyo kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo kwa kweli hoja yangu kubwa ni hiyo, kwamba muda umefika hili jambo lifanywe likamilike. Na tutumie fursa ambayo naisema kila siku; Mheshimiwa Rais amekuja na mambo hayo manne, suala la reform ni muhimu, kama kuna eneo la kufanya reform kubwa kuliko yote ni suala hili. Kwa saabu kwa kweli hata kama tunazungumzia Katiba mpya, itakapofika mjadala hili ni suala ambalo lazima tuliangalie kwa makini sana ili Watanzania haki zao za asili zilindwe popote walipo, iwe ni ndani ama nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwanza nimpongeze CEO wa Simba kwa kuwa na roho ngumu kuwepo humu ndani leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwenye Kamati yetu, niongeze sauti kidogo kwenye eneo moja la utamaduni na nataka kuzungumia umuhimu wa utamaduni. Kwa kweli utamaduni ni dhana muhimu sana katika kufikia Tanzania ambayo tunaitaka kimaendeleo. Changamoto nyingi ambazo tunakumbana nazo tungeweza kuzitatua kama tukizingatia dhana hii ya utamaduni. Mara nyingi tukizungumzia utamaduni watu wanazungumzia habari za sanaa, maigizo, nyimbo ngoma za asili, hizo ni sehemu muhimu, lakini sio utamaduni pekee, ni sehemu muhimu ya utamaduni, lakini haiwezi kuwa pekee yake, lakini muhimu ni kwamba utamaduni kwa kweli ni mtindo wa maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo yale mawazo, desturi, tabia ya kijamii, mkusanyiko wake ndio tunapata utamaduni. Kwa mfano, tunapozungumzia ubunifu, ili tuweze kuwa na ubunifu maana yake tunahitaji kujenga utamaduni wa ubunifu, kwa mfano kuwa na tabia ya kujaribu na kutokuogopa kukosea. Kama tukisema kupambana na rushwa, sheria pekee yake haitoshi, lazima tujenge utamaduni wa kukataa kwa mfano shortcut na ujanja ujanja katika Maisha, ni utamaduni. Ukiwa na jamii ambayo utamaduni wake ni ujanja ujanja, shortcut hata utunge sheria ngumu namna gani, bado rushwa itakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo utamaduni ni jambo la msingi sana katika kukamilisha ambayo tunayataka. Hata sasa hivi Mheshimiwa Rais anapanua mambo ya demokrasia, maridhiano na yenyewe inahitaji kujenga utamaduni wa kidemokrasia, ikiwemo utamaduni wa kupingana kwa hoja bila kuchukiana, utamaduni wa kustahimiliana tunapotofautiana na utamaduni wa kuheshimu sheria na haki za watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo utamaduni wa kuheshimu sheria ni muhimu sana, unaweza ukawa na sheria nzuri, lakini kama hamna utamaduni huo itakuwa ni changamoto. Kwa sasa hivi lazima tupongeze kwamba nchi yetu ina utamaduni mzuri kwenye michezo. Tuna timu mbili kubwa Yanga na Simba tunashindana, tunataniana, tunacheka, hatugombani, jambo jema ni utamaduni mzuri sana. Hata kama wenzetu ndio hivyo tena lakini tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kutokana na umuhimu wa utamaduni nchi yetu hii tangu tulipoanza, hotuba ya kwanza ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati huo Tanganyika kama Republic katika Bunge Mkutano wa Tano wa Bunge, tarehe 10 Desemba, Mwalimu Nyerere alitangaza kufanya mabadiliko makubwa mawili katika Serikali yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, badiliko moja ambalo alifanya aliamua kuanzisha Wizara Maalum ambayo wakati huo aliita Ministry of National Culture and Youth, baadaye wakatafsiri wengine wakaita Wizara ya Mila za Taifa na Uongozi wa Vijana. Kwa hiyo, ukienda Waziri wa kwanza wa Wizara hii alikuwa anaitwa Bwana Kundya, Mbunge wa Singida alikuwa anaitwa Waziri. Mheshimiwa Sima, Mbunge wako wa kwanza alikuwa Kundya huyo na alikuwa Waziri wa Mila za Taifa na Uongozi wa Vijana. Kwa hiyo, Mwalimu aliamua kuanzisha Wizara Maalum, baadaye wakafuata wengine akina Chedya na kadhalika, lakini hatimaye akaja Meja Jenerali Sarakikya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo kwa muda mrefu tukawa na hii Wizara na katika historia ya nchi yetu ni mara mbili tu tumekuwa na Wizara dedicated kwa ajili ya utamaduni na sanaa. Mara ya kwanza ni hiyo ilikuwa tarehe 10 Desemba, 1962, mara ya pili ni mwaka jana tarehe 8 Januari, 2022. Pale ambapo Mheshimiwa Rais aliamua kuunda Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo. Kwa hiyo, ni uamuzi ambao ni mkubwa na unaakisi malengo yale ambayo Mwalimu Nyerere aliyatanganza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale aliposema Makamu Mwenyekiti sisi Kamati hatuwezi kuelewa, katika kipindi ambacho Mheshimiwa Rais ameamua kufuata nyayo za Baba wa Taifa 1962 tukiwa watu milioni 10, inawezekanaje tumeunda Wizara Maalum watu milioni 61 halafu unapunguza bajeti ya maendeleo, hili haliwezi kueleweka. Kwa hiyo tuombe sana Serikali ilione jambo hili kwamba ni muhimu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niende katika jambo la pili, of course siwezi kumaliza hotuba yangu bila kuipongeza Timu ya Yanga kwa kazi kubwa ambayo wameifanya. Wameijengea heshima nchi, dunia imeona, nchi imeona, lakini Mheshimiwa Rais ameona jambo kubwa sana hili. Kwa hiyo, tunawapongeza na nadhani mambo mazuri huwa yanaigwa, nishauri kwa mfano, pale Dar es Salaam tuna Mkuu wa Mkoa pale, Albert Chalamila, mahiri sana, machachari, pengine angeweza kuamua wale ambao wamefika robo fainali awaandalie lunch ya Mkuu wa Mkoa pale. Kwa hiyo, mtu akiingia robo fainali Mkuu wa Mkoa anaandaa lunch, akiingia fainali dinner kwa Mheshimiwa Rais, tatizo liko wapi? Kwa hivyo jambo hili watu wasiwe na nani na nini, inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, pale Ubungo tuna mabingwa 30 wa ndondi, 30 Jimbo la Ubungo pekee yake kwenye mambo ya ngumi. Nataka niwapongeze vijana hawa na kwa niaba yao niwataje wachache tu kwa sababu ya muda. Nimtaje Binti yetu Amina Mohamedi, hongera sana; Mariam Macho, hongera sana; Iddi Pialali, hongera sana; Hassan Ndoga, hongera sana, Mfaume Mfaume, hongera sana kwa kazi kubwa ambayo ameifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wasanii wote kutoka Jimbo la Ubungo wanamuziki ambao walishinda tuzo za muziki nimpongeze sana kupitia kwake Ndugu yetu Dulla Makabila ambaye aliibuka kuwa msanii bora wa kiume wa singeli, hongera sana Dulla Makabila. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni ombi kwa Mheshimiwa Waziri, Dar es Salaam na hasa Wilaya ya Ubungo tuna mashindano ya Ndondo Cup. Tunayo maombi mawili, ombi la kwanza atusaidie sana Mheshimiwa Waziri, vile Viwanja wa Kinesi na TP ni viwanja muhimu ambavyo vinatumika kwa ajili ya mashindano ya Ndondo Cup, lakini havijakaa vizuri. Tumwombe sana, tena sasa Mwenyekiti anaaongea, amwangalie Mwenyekiti wake aweke kiwanja pale, jambo jema kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, suala la Ndondo Cup tunaomba liingie katika mfumo rasmi wa kiligi litambuliwe. Kwa sababu linaibua vipaji vya vijana wengi sana, otherwise Mheshimiwa Waziri sisi kama Kamati kama alivyosema mwenzangu tunampongeza kwa kazi nzuri, ana hamasa nzuri, juzi amewatia vijana wetu hamasa nzuri sana pale Algeria, ile tumeshinda lakini tumeshindwa kikanuni. Kimchezo tulishinda, lakini kikanuni tukashindwa, lakini Waziri amechangia sana kwa hamasa zako. Tunashukuru kwa hamasa kubwa ambayo Mheshimiwa Rais ameitoa, vijana wanawaka moto na tunaamini mwaka huu timu zetu zaidi ya mbili zitaenda vizuri katika Mashindano ya Kombe la Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Mkoa wa Dar es Salaam ndiyo Mkoa ambao una network ndogo ya TANROADS kuliko nchi nzima, tuna barabara 51 za TANROADS urefu wa kilometa 601. Katika Jimbo la Ubungo ndilo lenye barabara chache cha TANROADS kuliko nchi nzima. Nimefanya hesabu kwenye mtandao wa TANROADS. Tuna barabara tano tu za TANROADS zenye urefu wa kilometa 28.8. Vile vile tunayo barabara moja ambayo imekuwa kitendawili kwa muda mrefu, inaitwa barabara ya Kimara – Kinyerezi; ikipita Kimara, Mavurunza - Bonyokwa hadi Kinyerezi, kilometa nane. Tangu mwaka 2010, Rais wetu wa nne aliahidi kwamba barabara hii itawekwa lami.

Mheshimiwa Spika, na kwa heshima yake ikaitwa Kikwete Highway mwezi wa pili mwaka huu kwenye Bunge hili niliuliza swali la nyongeza hapa kwa Mheshimiwa Naibu Waziri na akanijibu vizuri sana niliuliza barabara hii itaanza kujengwa lini? Mheshimiwa Naibu Waziri akajibu kwa furaha na kwa ushujaa mkubwa kwamba barabara hii ingeanzwa kujengwa na mwaka huu ingewekwa kwenye bajeti.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Engineer Kasekenya, nimeangalia kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri nimeenda pale kilichonishangaza ni kwamba barabara hii miaka yote huwa inakaa kwenye kiambatisho cha 5(b)na kinakuwa sehemu ya A ambayo inakuwa ni barabara za lami safari hii imewekwa sehemu ya B ambayo ni barabara ya changarawe ama udongo.

Mheshimiwa Spika, sasa Mheshimiwa Naibu Waziri lile jibu lako liliibua shangwe pale Kimara, Kimara inawatu 118,000 ni sehemu muhimu sana Kimara ina baa peke yake 48 biashara rundo pale guest house 34, saloon 20, maduka rejareja 191, supermarket zipo 16 yaani pale ni eneo kubwa la biashara, watu wengi ikaibuka shangwe watu wakaanza kujiandaa kufungua biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa leo hii habari itasababisha mgutuko wa akili, mshtuko wa moyo na mtanziko wa kiroho, kwangu mwenyewe na kwa wananchi wa Jimbo la Ubungo na hususani Kata ya Kimara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili jambo naomba Mheshimiwa Waziri ulieleze vizuri na ningesema hapa nishike shilingi lakini Mheshimiwa Professor Mbarawa alikuwa bosi wangu alikuwa Waziri wa Maji nikiwa Katibu Mkuu wake nilimsaidia akaupiga mwingi mpaka mama amemuona tena kwenye wizara hii nyeti sasa Mheshimiwa Professor Mbarawa mimi si nilikusaidia pale ukaupiga mwingi pale wewe hii barabara kilometa nane ukimsaidia Katibu Mkuu wako kuna ubaya gani? yaani kweli Katibu Mkuu wako ashike shilingi haiwezekani kwa sababu Mheshimiwa Mkuchika alishanifundisha kwamba once a boss always a boss wewe ni bosi wangu sasa nitashikaje shilingi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hebu nisaidie hili peke yake tafadhali kilometa nane Kimara – Mavurunza – Bonyokwa – Kinyerezi watu 118,000 biashara chungu nzima wale wananchi walifurahi na nimeenda pale Kimara nimepokelewa kama mfalme nitaendaje sasa hivi? Nilikuwa napanga nikafanye mkutano wa hadhara nitafanyaje mkutano wa hadhara katika mazingira haya. Professor Mbarawa uniokoe bwana kauli yako tu hili linaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho; katika Mpango Wetu wa Maendeleo huu wa Tatu bado miundombinu kipaumbele cha juu na kwakweli mahitaji ya barabara bado makubwa kama ambavyo tumeona kwa Waheshimiwa Wabunge hapa lakini mwaka huu labda Mheshimiwa Waziri utoe maelezo kidogo mwaka huu wizara Sekta ya Ujenzi bajeti imepungua mwaka jana ilikuwa 1.588 trillion mwaka huu ni trilioni 1.42 kwanini bajeti imepungua ya Sekta ya Ujenzi wakati Bajeti Kuu ya Serikali imepanda trilioni 37 mpaka trilioni 41 nadhani Mheshimiwa Waziri atupe maelezo.

Mheshimiwa Spika, na mwisho nichukue nafasi hii anapo ingia kiongozi mpya anakuwa na kazi kubwa tatu kwanza; ni kuendeleza yale mazuri aliyoyakuta; pili ni kurekebisha yale ambayo yalijitokeza changamoto ambazo hazifai kwa kipindi hicho na tatu ni kuleta mambo mapya. Mheshimiwa Rais wetu kwakweli aliahidi angehakikisha kwamba miradi yote mikubwa inaendelea na tuchukue nafasi hii kumshukuru sana kwasababu miradi yote muhimu inaendelea kama ilivyo na kwa kasi zaidi hili ni muhimu tumpongeze na tumshukuru sana kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumtie moyo kwamba hii miradi tupo naye na itasimama na niwahahakishie nimefanya kazi na Mheshimiwa Professor Mbarawa ni mtu ambaye kwenye miradi anajua kuisimamia ila tu wewe muhimu kabisa Mheshimiwa nakutia moyo lakini barabara yangu ya Kimara – Kinyerezi iangalie ni muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, wanasaikolojia hueleza maana ya maisha kuwa ni mchakato wa binadamu na jamii yake kusaka na kutunza furaha, yaani tunafanya mambo yote haya ya maendeleo katika nyanja zake zote ili hatimaye tupate furaha kama mtu mmoja mmoja, jamii na hatimaye Taifa. Kiwango cha furaha katika nchi ni kigezo na kiashiria muhimu sana katika kupima ubora wa maisha katika jamii na nchi husika. Ni kwa sababu hii kila mwaka hutolewa taarifa ya dunia kuhusu kiwango cha furaha katika kila nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taarifa ya mwaka 2022 iliyotolewa na taasisi inayojihusisha na kupima kiwango cha furaha duniani ya Gallup World Poll wastani wa kiwango cha furaha katika nchi yetu kilikuwa ni 3.623 (kiwango cha juu ni 10.0), tukiwa ni miongoni mwa nchi kumi duniani ambazo watu wake wanaonesha kiwango cha chini cha furaha. Nchi zngine ni Burundi (3.775), Yemen (3.658), Tanzania (3.623), Haiti (3.615), Malawi (3.6), Lesotho (3.512), Botswana (3.467), Rwanda (3.415), Zimbabwe (3.145) na Afghanistan (2.523). Taarifa hii inapatikana https://dmerharyana.org/world-happiness-index/

Mheshimiwa Spika, ukisoma majukumu ya jumla ya Wizara hii utaona kuwa jukumu la msingi la Wizara hii ni kuweka mazingira mazuri kwa ajili ya kuleta furaha na kuamsha matumaini kwa jamii na kwa mtu mmoja mmoja. Na mimi katika mchango wangu ninataka nichangie maeneo mawili ambayo ninashauri Wizara ichukue hatua kadhaa za kisera na kisheria katika kuleta furaha kwa jamii yetu.

Kuhusu haja ya kinga jamii wa wazee; kwa kuzingatia makadirio ya idadi ya watu (population projections) ya NBS, Tanzania inakadiriwa kuwa na watu 61,280,743 na inatarajiwa kuwa na watu 67,036,280 ifikapo mwaka 2025. Kati ya idadi hii ya watu, wazee[1] ni watu 2,801,541 kwa mwaka 2022 (sawa na asilimia 4.6) na inatarajiwa kuwa 3,038,267 mwaka 2025. Hawa ni Watanzania ambao kwa nyakati tofauti waliwahi kuitumikia nchi yetu ama katika nafasi za kuajiriwa au kujiajiri au katika mashamba huko vijijini.

Mheshimiwa Spika, takwimu zinaonesha pia kwamba katika nchi yetu zaidi ya asilimia 80 ya wazee wanaishi vijijini na wakiwa huko wanalazimika kufanya kazi zozote ili waendelee kuishi. Wengi wao hawana msaada. Aidha, takwimu zinaonesha kuwa wazee ndio wanaotunza watoto yatima; asilimia 40 ya watoto yatima Tanzania wanatunzwa na wazee ambao nao wanahitaji kutunzwa.

Mheshimiwa Spika, takwimu nyingine muhimu ni kwamba ni asilimia 6.5 pekee ya wazee nchini Tanzania ndio wanaopokea malipo ya uzeeni (pensheni). Wazee walio wengi hawana msaada hasa kufuatia kuanza kuvunjika kwa mfumo wa familia jamii (extended family) kwenda katika mfumo familia ya kibaolojia (nuclear family). Aidha, tafiti zinaonesha kuwa kiwango cha umaskini kwa kaya zenye wazee nchini kipo juu kwa asilimia 22.4 zaidi ya wastani wa kitaifa!

Kutokana hali yao, wazee wengi wanakabiliwa na ukosefu wa usalama wa kifedha, wapo katika hatari zaidi ya kuugua magonjwa sugu, na wanakabiliwa na upweke.

Mheshimiwa Spika,nini kifanyike? Ninapendekeza tutekeleze kinga jamii (social protection for all). Mwaka 2010 Serikali ilifanya utafiti mzuri sana unaoitwa Achieving income security in old age for all Tanzanians: a study into the feasibility of a universal social pension. Pamoja na mambo mengine, utafiti ulipendekeza kulipa wazee kinga ya jamii kwa kiwango cha shilingi 16,586. Kwa bei ya leo hii inaweza ikawa sawa na shilingi 28,586. Kwa idadi niliyoeleza hapo juu hii ni sawa na shilingi bilioni 80 kwa mwezi sawa na shilingi bilioni 961 kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, nini faida ya kinga jamii kwa wazee? Katika mpango wetu wa maendeleo wa tatu wa miaka mitano (2021/22-2025/26), pamoja na mambo mengine, tumejiwekea lengo kuwa ifikapo mwaka 2025/2026 tuwe tumepunguza idadi ya watu maskini (wanaoishi chini ya mstari wa umaskini) kutoka watu milioni 26.4 mwaka 2020/2021 hadi watu milioni 20.2 mwaka 2025/2026. Lengo hili sio dogo kwa kuzingatia kuwa pamoja na kwamba uchumi uliendelea kukua vizuri hadi kufikia hatua ya uchumi wa kati wa chini, ukuaji huu haukwenda sambamba na kupungua kwa idadi ya watu maskini. Ukweli ni kwamba idadi ya watu maskini iliongezeka kwa watu takribani milioni mbili katika kipindi hicho.

Mheshimiwa Spika, faida za hatua ya kutoa kinga ya jamii kwa wote ni kubwa. Ukiacha kuongeza furaha kwa wazee wetu hawa, tafiti zinaonesha kuwa hatua hii itapunguza kiwango cha umaskini miongoni mwa wazee kwa asilimia 57.9. Aidha, hatua hii itasababisha kuwaondoa watu zaidi ya milioni 1.5 katika wimbi la umaskini wa kutupa. Kwa maneno mengine, hatua hii itasaidia sana katika kufikia malengo tuliyojiwekea katika mpango wetu wa maendelea katika kupunguza idadi ya watu maskini. Tayari nchi nyingi zimechukua hatua hii na matunda yanaonekana. Nchi jirani ya Kenya walitumia taarifa yetu ya utafiti na sasa wanatekeleza mpango huu. Nchi zingine Afrika ni pamoja na Mauritius, Lesotho, Afrika Kusini, Eswatini, Zambia, na Uganda wapo katika majaribio.

Mheshimiwa Spika, haja ya kuondoa zuio la kutafuta furaha wakati wa asubuhi na mchana; juzi nikiwa Dar es Salaam nilipata malalamiko kutoka kwa mmoja wapiga kura wangu kutika katika Kata ya Makubiri. Mpiga kura huyu ni daktari wa binadamu anayefanya kazi katika kitengo cha mortuary katika moja ya hospitali za Serikali katika Mkoa wa Dar es Salaam. Mara nyingi huingia usiku na kutoka asubihi. Kwa utaratibu aliojiwekea, kila anapotoka asubuhi hupitia baa iliyopo karibu na nyumbani kwake na kunywa bia sita kabla hajaenda nyumbani kulala. Alilalamika kuwa kila anapopita baa na kunywa hukamatwa na askari na huachiwa baada ya “mazungumzo”. Aidha, mwenye baa pia hukamatwa na kuachiwa katika mazingira hayo hayo.

Mheshimiwa Spika, siku ya Ijumaa tarehe 20 Mei, 2022 nilikutana na wafanyabiashara zaidi ya 200 kutoka katika Jimbo la Ubungo kwa lengo la kusikiliza kero na ushauri na kupokea maagizo yao kuhusu mambo ambayo wangependa niyawakilishe hapa Bungeni. Moja ya malalamiko makubwa yanafanana na ya daktari niliyemwelezea hapo juu kwamba wafanyabiashara katika jiji la biashara wanazuiawa kufungua biashara asubuhi na kuzuiwa kufanya biashara baada ya saa sita usiku! Baada ya kufuatilia na kuzungumza na baadhi ya Maafisa Biashara na maaskari wanaosimamia utaratibu huu, nimebaini kuwa tunayo Sheria ya Vileo (The Intoxicating Liquors Act, 1968) ya mwaka 1968. Katika kifungu cha 14, sheria imeweka muda wa kuuza vileo ambapo ni kuanzia saa sita mchana hadi saa sita usiku kwa siku za kazi. Ni wazi kuwa sheria hii imepitwa na wakati ukizingatia kuwa ilitungwa mwaka mmoja baada ya kutangazwa kwa Azimio la Arusha na wakati huo nchi ikijulikana kuwa ni nchi ya wakulima na wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, sasa ni muhimu sheria hii na zingine zinazopangia watu muda wa kufurahi ziangaliwe. Kawaida majiji duniani kote huwa yanafanya kazi saa ishirini na nne na kuna watu ambao wanafanya kazi usiku na kupumzika mchana. Tunaweza kuzipa mamlaka za Serikali za Mitaa zikatunga sheria ndogo kutokana na mazingira yao kulikoni kuendelea kuwa na sheria moja ambayo inakwaza sana biashara na kuondoa furaha za watu.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003, dhana ‘mzee’ hutafisiriwa kwa kuzingatia umri mkubwa, majukumu aliyonayo na hadhi ya mtu katika jamii. Katika maoni yangu haya ninazingatia umri wa mtu ambapo kwa mujibu wa sera hii mzee ni mtu yeyote mwenye umri wa miaka 60 na kuendelea. Kigezo kikubwa ni kwamba katika umri huu binadamu huanza kupungukiwa nguvu za kufanya kazi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Nataka nichangie pointi tatu tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nataka nitumie nafasi hii kuwapongeza sana, pale Jimbo la Ubungo kama unavyojua, tumejaliwa, tuna kila aina ya talent pale. Nataka nitumie nafasi hii niwapongeze vijana wetu, tuna timu pale za mpira wa miguu 25, karibu timu tatu kwa kila Kata, wanacheza na zimesajiliwa na TFF. Tunazo timu tisa za netiboli, wanacheza, pia pale tuna champions, wanamichezo wa ngumi, kila Kata, wako wengi. Tunao champions ambao wameshakuwa na majina Kitaifa, nataka niwapongeze sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza champion Selemani Kidunda wa kutoka Jeshi Camp kutoka Kata ya Mburahati. Champion Mfaume Mfaume wote mnamfahamu hapa, si mumpigie makofi, kutoka Kata ya Mabibo. Tunaye Champion Baiza Mazola kutoka Kata ya Mabibo. Champion Nasib Ramadhan kutoka Kata ya Mabibo. Champion Iddi Pialali wote tunamfahamu huyu kutoka Kata ya Manzese. Tunaye Champion Pengo kutoka Kata ya Manzese. Hawa ni vijana ambao wanatupa furaha sana kwa sababu Wizara hii moja ya jukumu lake ni kuleta furaha katika nchi na hawa vijana wanatupa furaha sana Dar-es-Salaam na katika kata yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze wanamuziki wakubwa, wazito katika Jimbo la Ubungo, nikianza na Dulla Makabila, anafanya vizuri sana. Shoko Mwamba anafanya vizuri sana. Madee Ali, kijana yule, Ney wa Mitego, Tundaman, Segu Segumbo, Dogo Dulla, Amigo, Bayo Fundi Ubungo na Mariam wote kutoka Ubungo. Wanaleta furaha katika Mkoa wa Dar-es-Salaam.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Wewe uliomba ruhusa kwenda hospitali, nenda hospitali. Hakuna taarifa, endelea. (Kicheko)

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Hoja yangu ya pili.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ester kaa chini wewe ni mgonjwa. Sasa usije ukazungumza vitu hapa. (Kicheko)

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni ombi. Nataka nichukue nafasi hii, Mheshimiwa Ester ugua pole, nataka nitumie nafasi hii nilete ombi. Pale Jimbo la Ubungo na hususan Kata ya Manzese na Sinza tuna uwanja wa kihistoria, uwanja unaoitwa TP. Huu ni uwanja ambao upo mpakani mwa Kata ya Manzese na Kata ya Sinza, Mtaa wa Chakula Bora upande wa Manzese na Mtaa wa Sinza E upande wa Sinza, ni uwanja muhimu sana na umuhimu wake pia ni wa kihistoria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla Yanga haijaanza mwaka 1935, mwaka 1920 mpaka 1926 ilikuwa inaitwa Young Boys na ilianzia Manzese kabla ya kwenda Kariakoo, walikuwa wanachezea uwanja huu wa TP. Baada ya kwenda Kariakoo ndio wakaanza kuitwa Young Africans na badaye mwaka 36 baada ya mambo kuwa mabaya walikuwa wanashindwa sana ndio wale jamaa wakajitoa wakaondolewa wakaenda wakaanzisha Simba. Kwa hiyo, Simba basically ni timu ambayo inatokana na Yanga, walikuwa ni waasi baada ya kufukuzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana maana haka kahistoria watu hawakaelewi, lakini ilianzia Manzese, ikaenda Kariakoo, 1935 ikawa ni Young Africans, 1936 wakaenguliwa baadhi wakaanzisha Simba, wakabaki Yanga kupigania uhuru, kwa hiyo, hili ni jambo la msingi. Sasa ule uwanja wa TP ni muhimu na tunahitaji kwa kweli kwa ajili ya…

NAIBU SPIKA: Sasa Mheshimiwa Kitila Mkumbo, Kiti kikikuomba ushahidi wa haya mambo unayo?

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ndio ninao, nitaleta. (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Haya, endelea.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nitaleta na paper zipo zimeandikwa, nitaleta. Ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aniangalie katika jambo hili. Kwa historia hii naomba anipe nguvu uwanja wa TP tuutengeneze, iweze kufanyika michezo. Sisi pale ni maarufu kwa suala la Ndondo Cup analifahamu, atatusaidia sana kwa Ndondo Cup.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho, kama nilivyosema awali, sisi maisha kisaikolojia, maisha ni nini? Ni mchakato wa kutafuta furaha, ndio maana ya maisha. Kwa hiyo, jambo lolote ambalo linaleta furaha ni muhimu likaungwa mkono. Sasa juzi nilikutana na, pia suala la furaha Mheshimiwa Waziri ni kazi yake, moja ya kazi ya msingi ya Wizara hii ni furaha. Nimeona hata kwenye speech yake ameiweka vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nimekaa na Daktari mmoja anafanya kazi katika moja ya hospitali za Serikali Dar-es-Salaam, yeye anakaa Kata ya Makuburi, amekuja kunilalamikia anasema karibu kila siku mara tatu kwa wiki anakamatwa. Kwa sababu gani? Yeye anafanya kazi mortuary, usiku anaondoka asubuhi. Kabla hajaenda nyumbani, ananiambia, yeye hunywa bia sita asubuhi, lakini kila akienda kunywa bia sita pale karibu na nyumbani kwake kwenye baa anakamatwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikakutana pia na wafanyabiashara, nilikuwa na kikao nao Dar-es-Salaam. Wakaniambia kwamba, Dar-es-Salaam moja ya lalamiko lao ni kwamba, hawaruhusiwi kufungua baa asubuhi na mwisho saa sita, kwa hiyo, inamaanisha kwamba, nikasema tatizo ni nini? Nikagundua kuna sheria ya The Intoxicating Liquors 1968, kile Kifungu cha 14, kimepangia watu muda wa kufurahi kwamba, hakuna kufurahi mpaka saa 6.00 mchana na mwisho wa kufurahi saa 6.00 usiku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wewe unafahamu majiji yote duniani hufanya kazi saa 24. Hii habari kwamba, watu asubuhi wasifungue biashara, wasifungue baa, wasifurahi mpaka saa 6.00 mchana ni sheria ya kizamani na hii sheria ilitungwa 1968 mwaka mmoja baada ya Azimio la Arusha ili watu na wakati huo nchi ilikuwa ni nchi ya wakulima na wafanyakazi, ilikuwa wanatakiwa wakalime mashambani, wakafanye kazi maofisini. Sasa huko tulishaondoka, hii ni nchi ya wakulima, wafanyakazi, wafanyabiashara, wanamichezo, wanaburudani, wote kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri aliangalie hili, hii sheria inazuia furaha ya nchi. Aiangalie tuibadilishe ili watu wawe na uhuru wa kufurahi wakati wowote maadam wanazingatia sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi...

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa. Mheshimiwa Gwajima.

TAARIFA

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nilipenda kumpa Taarifa tu rafiki yangu Mheshimiwa Profesa Kitila kwamba, furaha haiko aina moja, ziko aina nyingi sana za furaha. Kama hawawezi wakaipata furaha inayotokana na kunywa pombe, basi wapate furaha inayotokana na vitu vingine. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kitila.

MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu nimtaarifu Mheshimiwa Askofu kwamba, kabla hajaziponya hizo roho, lazima tuponye miili ili apate roho. Kwa hiyo na kwa sababu hiyo, naomba kwa heshima na taadhima nisipokee Taarifa yake. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, so, namalizia kwamba, on a serious note na hii baadaye Wizara ya Fedha itamhusu kwenye bajeti yake, Dar-es-Salaam Jiji la biashara, hawawezi kupanga muda wa kufanya biashara. Dar-es-Salaam watu watafanya kazi 24 Hours, mtu anafanya kazi usiku ana haki ya kwenda kufanya burudani asubuhi. Hii tuiangalie sheria hii ibadilishwe ili tufanye biashara 24 Hours tukusanye kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nichukue nafasi hii kabisa kwa dhati nimpongeze sana Mheshimiwa Mchengerwa. Nampongeza kwa jambo moja tu, hii Wizara ameipa hadhi sana, ameipa heshima, yaani ni Waziri ambaye yuko very proud kuwa Waziri wa Michezo, this is very good. Ameifanya kwamba, kumbe kila mtu anaweza akatamani kuwa Waziri wa Michezo, nampongeza kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. (Makofi)