Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. David Mwakiposa Kihenzile (15 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunipa nafasi hii hapa leo. Pia nimshukuru Rais wetu kwa ushindi wa kishindo, Mheshimiwa Waziri Mkuu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitumie nafasi hii ya leo kuchangia hotuba ya Mhesimiwa Rais, nimepata nafasi ya kuisoma, hotuba ni nzuri sana na inakwenda kuakisi sifa kuu za kiongozi, kiongozi sharti awe mcha Mungu, awe na maono na awe na utekelezaji wa haya ninayoyapanga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiisoma hotuba hii nitaangalia maneno machache, mfano ukurasa wa 26 unazungumzia viwanda, naomba nifungamanishe viwanda pamoja na miundombinu. Rais wetu ametupa sifa kuu tatu ya aina ya viwanda wanavyovitaka; moja, viwe ni viwanda ambavyo malighafi zake zinapatikana nchini; pili, viwe ni viwanda ambavyo vinatumika bidhaa zake na Watanzania walio wengi; lakini tatu, viwe ni viwanda ambavyo vinatoa ajira na alisema ikiwezekana asilimia 40 za ajira zote nchini zitokane na viwanda hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kweli tukiamua kujenga viwanda, kazi ambayo najua Mawaziri wetu mnaifanya vizuri sana lazima tuangalie maeneo ya kimkakati. Naomba nitazame kipekee eneo kama la kwetu pale Mufindi Kusini kuna viwanda zaidi ya tisa, kikiwemo kiwanda kikubwa cha Mgololo, barabara zake mpaka sasa hivi bado sio za lami, magari yanapita maelfu kwa kila siku na kodi tunalipa zaidi ya shilingi bilioni 40.

Mheshimiwa Spika, nadhani kama tunataka tukuze sekta hii tunapotazama maeneo ya barabara na mikoa, barabara za wilaya za nchi, lakini maeneo kama haya ambako ndiko kuna wale ng’ombe wetu ambao kimsingi wanatoa maziwa mengi, tutaweza kusaidia nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nipongeze pia kwa kazi kubwa ambayo imefanywa kwenye nishati, sote ni mashahidi vijiji vilikuwepo 2,108 vyenye umeme wakati huo leo vijiji 9,184 tulikuwa tunazalisha megawati 1308 leo tunazungumza megawati 1601. Tuna mradi mkubwa wa Stigler’s Gorge ambao unakwenda kutuzalishia karibia megawati 2115 hii ni kazi kubwa sana ambayo amefanya Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu maeneo yaliyobaki sasa ni vema Wizara ikaweka mkakati kwa kuzingatia maeneo matatu; moja, baada ya kukamilisha vijiji vilivyobakia vile sasa twende kwenye maeneo ya taasisi iwe ni mkakati kwamba kila shule, kila zahanati, kila ofisi ya kijiji ikawe na umeme, vitongoji vilivyobakia pia vikapate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda ni mdogo nigusie kidogo eneo la maji, maji ni uhai, tumeona na tumeshuhudia kipindi hicho ambacho kimsingi miaka mitano. Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli amewaza kumuvuzisha nchi kutoka kwenye asilimia 41 maji vijiji mpaka asilimia 70 sasa. (Makofi)

Ombi langu sasa tuongeze bajeti ikiwemo maeneo yetu ya Jimbo letu la Mufindi Kusini, ambapo kulikuwa na miradi kama ya Himayi, ilikuwa ni miradi mikubwa ili angalau tukapate maji kwa wingi zaidi. Sekta hii iongezewe maji kwa sababu kama ni wataalam inayo wazuri, Waziri wa Maji ni mzuri, mchapakazi, anakesha kwenye site, na tukitatua tatizo la maji Watanzania walio wengi zaidi watakuwa wameanza kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ningependa kuzungumzia ajira. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo, ametueleza kwamba atakwenda kuunganisha mifuko 18 ya vijana na ndiyo ilikuwa kazi ya kwanza aliyomkabidhi Waziri wetu Mkuu akaifanye, pamoja na jambo hilo lakini naomba tukatazame kwenye mitaala yetu. Je, mitaala tuliyonayo ina reflct mahitaji halisi huko mtaani? Hatusemi kwamba kusoma zinjanthropus na sokwe sio jambo baya, lakini kama vijana wanakwenda kujiajiri kwenye kilimo, pengine kwenye ujasiriamali, kwenye biashara, hayo ndiyo masomo ya lazima kwa sababu walio wengi wanakwenda huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutazame pia kwenye sekta ya utalii sote ni mashahidi nchi yetu hii mwaka 2015 watalii waliokuwa wanakuja nchini ni milioni 1.2 leo wako milioni 1.5 mkakati ni kupata watalii milioni tano ikifika mwaka 2025.

Tumetoka kwenye kupata dola za kigeni karibu bilioni 2.6 leo tunakaribia bilioni sita, lazima tunapofikiria kupata watalii milioni tano tutazame maeneo mengine kwa sababu leo karibu asilimia 80 ya watalii upande wa Kaskazini, hapa tuna Mbuga yetu ya Ruaha...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi na pengine nipongeze kazi kubwa ambayo unafanya na wenzetu kuanzia Waziri mwenyewe pamoja na majeshi yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ilitaka tu kuongelea kwenye maeneo machache lakini moja wapo wa maeneo nataka kuzungumzia ni mazingira ya kazi kwa wenzetu wa Jeshi la Polisi. Ni vyema Serikali ikatazama kwa kina mazingira yale ya kazi, leo ukiingia kwa OCD au ofisini pale Polisi wakati mwingine mazingira hayatoshi, furniture ni za hovyo. Ni vizuri tukalitazama hilo ili kulipa heshima Jeshi letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili tumeona jinsi ambavyo tumekabidhi dhamana kwa wenzetu wa Jeshi la Polisi, wanafanya kazi kubwa ya usalama wa nchi yetu. Na hili nafikiri Mheshimiwa Waziri ni vizuri ukalitazama vizuri sana hili tutakapokuwa tunapitisha huko baadaye kwasababu haiwezekani Polisi wanafanya operesheni za ulinzi na usalama wa watu wetu na sisi kipaumbele cha kwanza ni ulinzi na usalama wa watu wetu na mali zao halafu OCD, OCS, wanaomba mafuta kwa wadau ambao miongoni mwao watageuka kuwa wahalifu, heshima ya Jeshi iko wapi hapo? Hii sio sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka kupendekeza tuweke mkakati mzuri ili kulipa heshima jeshi letu angalau wanapofanya shughuli zao wawe na bajeti ya kutosha. Tunawapa inferiority complex n ahata uwezo wa kusimamia sheria na kanuni inakuwa ni changamoto.

Pili, tunajikuta tunalazimisha vitendo vinavyoitwa rushwa, yue mtu anawapa mafuta kila siku, kesho unakuja kumuambia ni mhalifu, kibinadamu inakuwa ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa wenzetu wa Jeshi la Polisi iko changamoto kubwa sana kwenye dhamana. Ni vyema mkalitazama nchi nzima kwenye vituo vyetu. Mfumo wetu wa utoaji dhamana ukoje? Kwa nini mtu akikamatwa Ijumaa anakaa mpaka Jumatatu wakati Jumamosi na Jumapili kazi inafanyika, tunafanya haya yote kwa faida ya nani? Ni vyema tukalitazama jambo hili pia kwa kina ili kusaidia watu wetu. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa hii ya kuweza kuchangia katika mjadala unaoendelea. Pengine nitajikita zaidi kwenye hoja ile ambayo inazungumzwa ya ongezeko la gharama kwenye lot 3 na lot 4 na nafasi ikitosha, basi nitaendelea na mengine.

Mheshimiwa Spika, moja ya hoja ambayo imezungumzwa ni kwamba, tulipotumia single source, taarifa yetu ya uchukuzi, tulipotumia single source gharama zilizongezeka by 1.3 million na 1.6 million per kilometer. Kabla sijaanza hata kujibu au kuingia kwenye kuchambua, logic pia nyepesi kabisa, unapojenga mradi mbali kutoka Dar es Salaam, unapoenda mbali zaidi gharama za usafiri na vitu vingine zinaongezeka. Hiyo ni kwa lugha nyepesi kabisa, lakini kwa kuwa imezungumziwa hoja ya kwamba ni kinyume na sheria za manunuzi, napenda pia kuzungumzia kwenye sheria yetu ya manunuzi Na. 7 ya mwaka 2011 na kanuni zake ambayo imetoa fursa na mazingira gani unayoweza kutumia single source.

Mheshimiwa Spika, ukienda Kifungu cha 161 (c), imeeleza kwa kirefu sana, lakini mojawapo ni kwamba, pengine kama mtu huyo yupo site au mmeona kuna faida kubwa ya kufanya hivyo. Tayari mkandarasi aliyekuwa anajenga lot 1 na 2 moja alikuwa site, pili alikuwa na mitambo, tatu Mradi wa lot 3 na 2 alikuwa ameshafika asilimia 97 na 95 respectively. Kwa hiyo, kwa wakati huo ilikuwa ni muhimu pengine kumtumia.

Mheshimiwa Spika, pengine wakati naendelea na hilo, kabla hatujachambua lot No. 3 na No. 4, hebu tuchambue gharama za lot No. 1 na No. 2 zimefanana ili tuweze kujenga hoja kumbe gharama za Na. 3 na Na. 4 kwa nini ziliongezeka? Ukienda kwenye Na. 1 na Na. 2 zilitofautiana kwa karibu dola 500,000 na sababu zilikuwa ni nyingi. Lot No. 1 inatoka Dar es Salaam mpaka Morogoro, ya pili inatoka Morogoro mpaka Makutupora. Na. 1 haikuwa na mahandaki, lot No. 2 ilikuwa na mahandaki karibu kilometa tatu. Hivyo usingetegemea zifanane. Pia, lot No. 2 vis-a-vis No. 1 ilikuwa inapita kwenye Mto Kondoa, kwa ambao ni wenyeji, pembezoni, jambo ambalo litakutaka katika eneo kubwa sana ujenge madaraja. Sasa katika hali hiyo, kama namba I na II hazikufanana, kwa nini tuseme Na. 3 na Na. 4 zifanane?

Mheshimiwa Spika, Na. 3 na Na. 4, tofauti za bei, it is very obvious, yako mambo kama 11, lakini kwa sababu muda leo ni mdogo naomba nitaje machache:-

Mheshimiwa Spika, nilisema na jana lot No. 3 na No. 4 inategemea kupita kwenye rift valley karibu kilometa 50 wakati lot No. 1 na 2 haina bonde la ufa. Gharama zitatofautiana. Lot No. 3 na No. 4 zina junction kubwa ambapo pale tunajenga karakana yetu, lakini pia tunakwenda kujenga Chuo cha Reli Tabora, center ya excellence ya Reli itakayohudumia karibu nchi zote za Afrika. Katika hali ya kawaida haiwezi kufanana na Lot No. 1 na No. 2 ambako kitu hicho hatuna.

Mheshimiwa Spika, ukiacha hilo, tunakwenda kujenga kituo kikubwa cha mizigo ambacho kinaunganisha karibu pande tatu. Kinaunganisha upande wa Dar es Salaam, reli inayokuja Dar es Salaam, inayokwenda Kigoma na inayokwenda Mwanza. Hii kwenye lot No. 1 na No. 2 hazipo. Ni vizuri Watanzania wakafahamu katika mazingira hayo haziwezi kuwa sawa.

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, eneo la Malongwe na Nyahua, wenyeji wa hapa wapo watanisaidia, karibu kilometa 40 inapita kwenye swamp. Huwezi kufananisha reli unayoijenga kutoka Dar es Salaam kupitia Pwani na ambayo inapita kwenye swamp. Kule kwenye swamp utajenga madaraja, utajenga makalavati, utainua matuta, kwa nini tunafikiri kwamba gharama zitakuwa sawa sawa? Ni vyema Watanzania wakalifahamu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, kati ya Salanda na Manyoni kuna miinuko miwili…

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa David Kihenzile, kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mpina.

Mheshimiwa Naibu Waziri, kaa kidogo.

TAARIFA

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, la kwanza, haya yote anayoyaongea Naibu Waziri, Mheshimiwa Mkaguzi wetu aliyakataa.

Mheshimiwa Spika, la pili, anachozungumzia kuhusu suala la mazingira ya mradi wa kutoka Morogoro kuja Makutupora…

SPIKA: Mheshimiwa Mpina, Taarifa ni moja.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, basi niiweke hiyo moja.

SPIKA: Haya, ahsante.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, hiyo moja …

SPIKA: Aah, umeshasema ya kwanza.

MHE. LUHAGA J. MPINA: Aah, ahsante.

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa David Kihenzile unaipokea Taarifa hiyo?

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, namwomba tu aendelee kunisikiliza kama nilivyokuwa namsikiliza huko nyuma. Taarifa yake naikataa, kuweka record vizuri. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Sawa. Sasa ngoja niweke sawa.

Waheshimiwa Wabunge, hoja hii ni ya Kamati zetu tatu. Waheshimiwa Mawaziri na Naibu Mawaziri kwenye hoja hii ni wachangiaji kama mchangiaji mwingine. Kwa hiyo, inaruhusiwa kutoa Taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa David Kihenzile.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, kwa sababu muda ni mdogo, naomba niseme jambo moja muhimu sana kwa kuhitimisha kabla sijaendelea pengine.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, engineering estimate ambazo zinatumika kwenye mradi huu zilifanywa kati ya 2012 na 2016.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Ngoja. Mheshimiwa Halima, sasa hapo utakuwa unanipa mimi Taarifa kwa sababu, ndiye niliyetoka kuzungumza.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, alikuwa ameshaanza.

SPIKA: Ngoja achangie halafu utapewa, maana la sivyo, utakuwa unanipa mimi Taarifa.

Mheshimiwa Kihenzile.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nilitaka niwarejeshe Waheshimiwa Wabunge…

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: …kwenye Ripoti ya International Union of Railways, yaani Taarifa ya Reli Duniani. Ni vizuri tukaelewana hapa, tukasikilizana kwa faida yetu sisi kama Wabunge pamoja na Waheshimiwa wananchi.

MHE. HALIMA J. MDEE: Kumbe inauma!

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, katika ripoti hiyo, imeainisha na ninaomba tutembee kifua mbele Watanzania; imeainisha Barani Afrika zimejengwa kilometa 7,200 katika hizo, 2000 ni za Tanzania. Katika mchanganuo…

SPIKA: Haya, Mheshimiwa Kihenzile kuna Taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Halima Mdee.

TAARIFA

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, kuhusiana na SGR na kwa mujibu wa mahojiano ambayo Kamati ya PAC imefanya kuhusiana na SGR, tumeambiwa wazi kwamba, mlilazimika kumpa mkandarasi Yapi Markezi, huyo Mturuki kwa sababu ya masharti ya Benki ya Standard Chartered. Masharti ya mikopo ndiyo yamewalazimisha mfanye maamuzi ambayo hayana maslahi. (Makofi)

SPIKA: Taarifa ni moja Mheshimiwa.

Mheshimiwa David Kihenzile, unaipokea Taarifa hiyo.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, Taarifa hiyo ninaikataa kwa sababu, haipo sehemu ya mjadala wangu. Tulimpa huyo baada ya kujiridhisha na vigezo vya Kitaifa. (Kicheko/Makofi)

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ninaendelea kwa sababu, nimekuwa Mwenyekiti, huwa ninafahamu taratibu na Kanuni.

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kuweza kuniruhusu. Nataka nitoe taarifa ya hali ya ujenzi wa reli Barani Afrika.

SPIKA: Mheshimiwa Waziri ngoja.

Mheshimiwa Anatropia, unatakiwa usubiri kidogo kwa sababu, sasa utakuwa unampa Taarifa juu ya nini? Maana la sivyo, utakuwa unampa Taarifa Mbunge mwenzio. Kwa hiyo, unamwacha achangie kidogo ndiyo umpe Taarifa kwenye hiyo hoja yake.

Mheshimiwa David Kihenzile.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nilitaka kuzungumza kwamba, katika kilometa 7,200 karibu kilometa 2,000 zimejengwa Tanzania. Mataifa mengine wanakuja kujifunza tumefanyaje Watanzania?

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, katika gharama, Tanzania tumejenga kwa gharama ndogo ya shilingi 4.3 million per kilometer. Nchi nyingine ni kama ifuatavyo: Nigeria 6.1 million, Kenya milioni 7.3, Ethiopia milioni 5.9, Morocco 6.5 million, sisi ni 4.3. Tutembee kifua mbele tujisifu, Mheshimiwa Rais Samia anatuongoza vizuri. Huko tunakoenda ni kuzuri zaidi. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kihenzile kwa sentensi yako naona hujamaliza, nataka kukuongeza dakika moja ili umalizie mchango.

Mheshimiwa Anatropia, Taarifa gani?

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa Taarifa, hoja ya CAG ni ku-award kandarasi bila kufanya ushindanishi, single source. Single source ambayo angepaswa kuifanya ingekuwa na economic value. Mkaguzi amejiridhisha kwamba, ame-award bila kuwa na economic value. Hiyo ndiyo hoja yetu.
SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa Kihenzile, dakika mbili, malizia mchango wako na kama unaikubali hii Taarifa au hapana.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Taarifa ninaikataa kwa sababu nimeshasema mwanzoni kwamba sheria inaruhusu. Tunaongelea sheria ya nchi. Kama nchi saba zimejengwa kilometa 7,200 na zinakuja Tanzania kujifunza tumejengaje kwa 4.3 dola kwa kilometa moja, kwa nini Watanzania tusijivunie mambo mazuri?

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Kwa nini msiyafurahie?

Mheshimiwa Spika, tutembee kifua mbele kwa sababu tumejenga reli kwa gharama ambazo ni nafuu ukifananisha na wengine. Hilo ni moja. Pili, engineering estimate ambayo tumejengea reli zetu iko chini. Kwa mfano, wakati engineering estimate ya lot No. 3 ilikuwa ni 4.9, tumejenga kwa 4.05 wakati ile ya lot No. 4 ilikuwa ni 4.8 tumejenga kwa 4.3. Kwa hiyo, tuko vizuri, tutembee kifua mbele, tujidai, miradi iko kimikakati, wengi wangetamani kuwa kama sisi, tujivune, tuchape kazi. Tumuunge mkono Rais wetu. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii pia kumshukuru Mwenyezi Mungu, wapiga kura wangu wa Jimbo la Mufindi Kusini na chama changu kwa heshima ya kunifikisha hapa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie kwa ufupi mambo machache juu ya Mpango ambao umewasilishwa vizuri sana na Mheshimiwa Waziri. Eneo la kwanza napenda kupongeza Mpango uliopita kwani tumefanya vizuri sana kwenye eneo la diplomasia. Tumefanya vizuri sana kwa maana tumeona matokeo makubwa kama vile unaona sasa uanzishwaji wa zile Kampuni ya Twiga ambapo Serikali ina asilimia 16, bomba la mafuta la kutoka Hoima – Tanga, haya ni matokeo ya sera nzuri sana ya diplomasia ya uchumi na usimamizi makini wa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo hili naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha Mpango atusaidie. Tunafanya kazi nzuri sana ya kuhamasisha watu wa nje kuja kuwekeza nchini, ni upi mkakati sasa wa sisi Watanzania kuhamasisha wafanyabiashara wetu, kuwapa mikopo na ruzuku waende wakawekeze kwenye nchi zingine? Tungetamani kuona magazeti yetu, vyombo vya habari vyetu na kampuni zetu, kama Clouds na wengine wanakwenda kwenye nchi zingine za nje ili kuweza kuongeza uwekezaji na mapato kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili napenda kuchangia kwa ufupi sana kwenye eneo la kilimo. Tunafahamu asilimia 7 ya ardhi ya China wanaitumia kwenye kuzalisha asilimia 22 ya mazao duniani. Sisi kwetu sekta hii inatusaidia kwa asilimia karibia 63 na mimi nijikite kwenye mazao makuu mawili ya chai na parachichi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba katika mazao ya kimkakati ambayo yametajwa ni vyema tukaweka na sheria kabisa ili kuyatambua na kuyawekea ruzuku maalum. Kwa mfano, kwenye zao la chai ambapo moja kati ya wilaya zinalima ni pamoja na kwetu kule Mufindi Kusini. Ukitazama kwenye zao la chai sisi hapa kama Tanzania tumezalisha karibia tani 37,000 lakini tunazouza nje ya nchi ni kidogo sana. Wenzetu Wakenya wanazalisha karibia tani 432,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza najiuliza, pamoja na diplomasia yetu nzuri katika masoko ya dunia, ni kwa nini chai yetu inapelekwa kwa kiasi kidogo nje ya nchi? Changamoto ni nini?

Kwa hiyo, napenda Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atusaidie pia Mpango wa kuweza kusaidia zao kama la chai ili ikiwezekana zitolewe pembejeo kwa wakulima, wahamasishwe watu wa kuweka viwanda vya kutosha katika eneo hili lakini zaidi ya yote mkakati wa namna ya kutoa huduma za ugani kwa sababu ndizo zinazoongeza gharama kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ni eneo la parachichi. Naomba zao hili liingizwe katika mazao ambayo tunayaita ni ya kimkakati kwenye nchi yetu. Kwa Mikoa kama Mbeya, Njombe mpaka Iringa ni zao ambalo tunaliita green gold yaani dhahabu ya kijani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi hapa tunapeleka nje ya nchi tani 8,500. Wenzetu Wakenya peke yao walipeleka tani 68,000 ikawaingizia pesa za kigeni dola milioni 128 lakini ukiichimbua zaidi sehemu kubwa zimetoka nchini kwetu. Ni upi mkakati wa Wizara, kwa sababu hapa haiwezekani maparachichi yanatoka kwenye maeneo yetu yanapelekwa Kenya halafu yanakwenda nje ya nchi inaonekana Kenya ndiyo inazalisha kwa kiasi kikubwa zaidi, shida ni nini?. Napenda kwenye majibu ya Mheshimiwa Waziri anisaidie kwenye eneo hili pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitazama China asilimia 40 ya soko la China, Kenya ndiyo wanapeleka lakini sisi tunafahamu kihistoria, Tanzania mahusiano yake na China ni makubwa kuanzia uhuru. Tunakosea wapi? Kwa nini watuzidi kete? Ukifuatilia nchini kwetu miradi ya ujenzi wa barabara na ya maji, kampuni za China zimejaa hapa. Kwa nini diplomasia yetu ya uchumi isitusaidie kupeleka mazao kama haya kwao, urafiki wetu una faida gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni kwenye viwanda. Kwanza napenda kuomba maeneo ambayo ni nyeti kwenye viwanda kama Mufindi Kusini yatangazwe kama ni ukanda maalum wa viwanda ili pengine msukumo wa kipekee uweze kuwekwa. Nimefurahi commitment ya Serikali asubuhi ya leo na kwa kweli nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi alipotamka kwamba katika bajeti itakayokwenda kuanza sasa tutakwenda kujenga barabara ya Mtwango – Nyololo kilometa 40, Mafinga – Mgololo kilometa 75.6. Barabara hii…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, kengele tayari.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kushukuru kwa Mpango huu ambao umeandikwa vizuri sana. Nitajikita kwenye sekta moja tu ambapo nizungumzia mahusiano kati ya Mpango hu una Sekta ya Ujenzi. Kabla sijafika huko, labda nimnukuu mmoja wa waasisi wa Marekani aliyekuwa anaitwa Benjamin Franklin ambaye aliwahi kutuambia kwamba failing to plan is planning to fail, unapokosea kupanga, basi unapanga kushindwa.

Mheshimiwa Spika, niungane kwanza na mtangulizi mmoja aliyezungumza pale juu kwamba tuweke mfumo mzuri wa kufuatilia, je, tunayokubaliana hapa yanatekelezwa? Mambo ya kimkakati na yenye tija sana yanapewa uzito sawa na Wabunge tunavyopendekeza? Hilo nataka iwe kama angalizo.

Mheshimiwa Spika, ukisoma Mpango katika maeneo ya kipaumbele, eneo namba mbili linazungumza linasema; kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani na utoaji wa huduma. Pia ukienda kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wetu, kwenye malengo mahsusi, namba tatu anasema:

“Kujenga uchumi wa viwanda kama msingi unaoongoza mauzo ya nje ili kuimarisha Tanzania kuwa kitovu cha uzalishaji katika nchi za ukanda wa Afrika Mashariki, SADC na Central.” Mwisho wa kunukuu.

Mheshimiwa Spika, tumekubali, tumeamua kujenga nchi ya viwanda. Lazima pia tunapotamka hilo tukubaliane, tunatamka viwanda kama theories au tunatamka viwanda kiutendaji. Nitajikita kwenye maeneo machache kama nilivyosema na pengine labda ningeshauri na Wabunge wakasome tafiti ya mtu mmoja anaitwa Peter Samuel Abdi ambaye anasema anahusianisha infrastructure na Industrialization, jinsi vitu hivi vinavyokwenda pamoja. Naomba nijikite kwenye ukanda wa viwanda. Kama tunataka nchi yetu twende kwenye viwanda na mwaka 2015 hapa wakati Hayati anahutubia alisema angependa kuona mwaka 2020, Sekta ya Viwanda itoe asilimia 30 ya ajira. Tulipofanya tathmini mwaka jana tukabaini asilimia nane inatokana na ajira kwenye viwanda. Hakuna anayejiuliza, hii asilimia 22 tumekwama wapi? Naomba niende kwenye kesi ya upande kwa mfano wa viwanda pale Mufindi.

Mheshimiwa Spika, pale Mufindi ikiwa inawakilisha sehemu zingine za nchi hii, maeneo ambayo yamejitenga yenyewe kuwa ya viwanda pale kuna viwanda karibu 10 na viwanda hivi viko kuanzia miaka ya 1961 vilianza. Vinalipa kodi zaidi ya bilioni 40 takriban, naweza kukutajia kwa uchache. Kuna Kiwanda cha Karatasi, hiki kinatengeneza karatasi hapa nchini kwetu na kupeleka nje. Kuna Viwanda vya Nguzo, kuna Viwanda vya Chai vimekusanyana pale. Sasa niwaombe wenzetu wa Sekta ya Ujenzi Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi yuko pale, Mheshimiwa Waziri wa Fedha yuko pale; maeneo kama haya ambayo wakiyakusanya yanaweza kuingizia Taifa bilioni 40, lakini tunayasoma kwenye takwimu pia kwamba katika miaka hii, kati ya viwanda 23 vya mbao peke yake, viwanda karibu 23 kati ya 27 vilikufa, hakuna anayejiuliza sababu ya kufa ni nini? Ningemwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha na timu yake walifanyie tathmini jambo hili.

Mheshimiwa Spika, pia tunaposema tuimarishe Sekta ya Viwanda kama msingi wa kuongoza nchi yetu, tunamaanisha magari yanayopangana barabarani zaidi ya 200 kila siku kipindi cha mvua, yatapita kiurahisi, utasafirisha bidhaa zako kutoka kiwandani mpaka nje. Kumbuka viwanda hivi vinapeleka bidhaa ndani ya nchi yetu na nje ya nchi yetu. Unahangaika kuanzisha viwanda vingine wakati vile vilivyopo mahitaji yake 50 ikiwemo barabara hujajenga, are we serious? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu, kwa kuwa agenda ya viwanda iliasiisiwa na Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Kwa kuwa, iliendelezwa na watangulizi wake mpaka Mheshimiwa Mama Samia sasa, Rais wetu wa Awamu ya Sita. Na kwa kuwa maeneo kama yale yametajwa kwenye Ilani ya CCM ninaomba tuyape kipaumbele ikiwezekana tuimarishe miundombinu yake, tujenge barabara, tupeleke umeme, tupeleke maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilifanya siku moja ziara pale, unamkuta mwenye kiwanda anasema bwana mimi hapa kodi inayolipa ni dola milioni mbili karibu nukta mbili, lakini shida yangu kubwa tazama huko nje hali ilivyo mbaya, sina barabara, anakwambia lakini umeme hapa ndani hautoshelezi.

Mheshimiwa Spika, sasa ombi langu, kwa kumalizia. Kwa kuwa, maeneo kama haya yametajwa kwenye Ilani ya CCM kuanzia 2005 mpaka sasa. Kwa kuwa, Mwalimu Nyerere aliahidi. Kwa kuwa, Rais Kikwete alirudia, kwa kuwa, baba yetu hayati Dkt. Magufuli ameyazungumza tena mwaka jana. Namna nzuri ya kuwaenzi viongozi hawa ni kuanza kutenda kusema inatosha. Tutakuwa na mipango hapa, tunakaa hapa ndani tunazungumza utekelezaji hauonekani wa baadhi ya maeneo. Kimshingi maeneo ambayo sisi huku nje tunakuwa hatuelewi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inawezekana labda kuna maelezo mazuri kama kwa kutumia msemo wako. Kunaweza kuwa na maelezo mazuri sana ya kwamba, barabara hizi hatuwezi kuzijenga kwasababu hizi na hizi na hizi, lakini sisi hatuelewi. Eneo hili limeajiri watu karibu elfu kumi, eneo hili linalipa kodi zaidi ya bilioni 40, eneo hili magari yanayopita na ajira pengine, n.k. shida ni nini?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa kuhitimisha ninaunga mkono hoja, lakini naombeni maeneo ya kimkakati tuyatazame kwa njia ya kipekee. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mzungumzaji wa kwanza jioni hii. Kwanza nishukuru Wizara chini ya Mheshimiwa Waziri na Manaibu wake na Makatibu Wakuu kwa sababu tunawafahamu record yao ya uchapakazi, tunaamini watakwenda kufanyia kazi changamoto zote ambazo ziko pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo machache. La kwanza iko changamoto kwenye Halmashauri zetu, pesa hazitoshi, ikifika karibu na mwisho wa mwaka tunaambiwa pesa zimerudishwa, shida ni nini wakati mahitaji yapo na miradi bado haijakamilika? Tunamuomba Mheshimiwa Waziri atusaidie jambo hili lisijitokeze. Kama changamoto ni fedha zinachelewa kupelekwa, basi angalau ziweze kutumwa katika muda muafaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, tunayo changamoto ya miradi ambayo haiishi. Akipita huko kwa navyofahamu uchapakazi wa dada yetu atapata nafasi ya kufanya survey kutazama miradi gani ilianza lini na kwa nini haijakamilika. Mimi nimefanya ziara kule kwangu kuna miradi mingine ina miaka mpaka 10 haijakamilika, hii si sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo napenda kuzungumzia ni la kupima ardhi, wananchi wanahitaji sana wapimiwe ardhi yao. Kwanza inaondoa migogoro, pili ni chanzo cha mapato cha uhakika cha Serikali yetu. Napenda Mheshimiwa Waziri anapokuja hapa kwa ajili ya kuhitimisha atuambie mpango wa Wizara suala hili wanalianzaje na pengine watalikamilisha lini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine ni changamoto ya ofisi zetu za Wakuu wa Wilaya. Katika mwongozo wa kuandaa bajeti tunaambiwa agenda namba moja ni suala la ulinzi na usalama. Hata hivyo, ukitazama Ofisi za Wakuu wa Wilaya kirasilimali zina changamoto kubwa sana. Mimi nashauri kwa kuwa ofisi za Wakuu wa Wilaya ndiyo wasimamizi wa Halmashauri Mheshimiwa Waziri atazame kama inawezekana asilimia sehemu ya mapato ya ndani iwe allocated kwa ajili ya kuendesha ofisi za Wakuu wa Wilaya kwa ajili ya mafuta na vitu vingine vidogo vidogo, tutawasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, agenda nyingine ambayo imezungumzwa na watu wengi hapa ni TARURA, ni changamoto kubwa sana. Suala hili naomba Mheshimiwa Waziri alichukue kwa namna tofauti. Barabara zikiwa mbovu zina uhusiano wa moja kwa moja na mapato hafifu ya Halmashauri. Barabara zikiwa mbovu zinaharibu magari ya Halmashauri, sasa kumbe kwa kuwa TARURA imewekwa ndani ya TAMISEMI, kama Serikali Kuu haiwezi kuongeza fedha basi ni vema ikatoka circular kwamba asilimia fulani ya mapato ya Halmashauri iende ikasaidie TARURA, Wakurugenzi wapewe na CAG anapokagua atazame, je, to what extent jambo hili limefanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo maalum kule kwangu, tunazo changamoto kwenye baadhi ya maeneo; mambo kama mawili hivi. Moja, Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anajibu au itakavyompendeza, naomba atusaidie vituo vya afya kwenye maeneo ambayo ni yako very critical. Mfano, tunayo Kata ya Mtwango ambayo waliojiandikisha kupiga kura ni zaidi ya 17,000, kumbuka Jimbo langu ni la vijijini lakini pale hakuna hata kituo cha afya na pembeni yake kuna kata zingine zaidi ya tatu, ikiwezekana na ikimpendeza atupatie vituo vya afya maeneo ya Mtwango, Idete na Itandula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vivyo hivyo kwenye upande wa ambulance, tunazo changamoto kubwa sana kuanzia eneo hilo lakini eneo lingine ni ukanda wa Mgololo ambako kuna kata karibia tatu na kuna kituo cha afya kimoja. Eneo lile hata nikikutumia picha hapa barabara ni mbovu, kuna kiwanda kikubwa cha karatasi kule kina wananchi zaidi ya 40,000 kwenye eneo lile, kuwatoa wagonjwa kule mpaka makao makuu ni changamoto kubwa mno, wakipata gari ya wagonjwa tutakuwa tumewasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo naomba kuchangia ni issue ya Taasisi zinazo-operate katika nchi yetu. Kwanza, nchi nyingi kama ni International NGO inakwenda kwenye nchi husika cha kwanza unapewa condition lazima ushirikiane na NGO au Institution iliyopo pale ndani. Kwanza hiyo ina ensure security kuwa monitor wale watu wakifika hapa wanafanya nini. Hapa kwetu kuna changamoto kidogo, nimuombe Mheshimiwa Waziri aweke mkakati mzuri zaidi, kama ni USAID au whatever wakifika washirikiane na taasisi za hapa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kutumia mfano mmoja, ni declare interest mimi ni Rais wa Red Cross, taasisi ya Kitanzania na inafanya kazi ya Watanzania, imeanzishwa kwa sheria ya Bunge na ikitaka kufutwa itafutwa Bungeni. Hata hivyo, kuna changamoto, kuna programu ambazo ilitakiwa izifanye yenyewe inafanya taasisi za nje matokeo yake wale hawawezi kuwa na uchungu; kama ni kutibu watu hawawezi kuwa na uchungu kama walivyo Watanzania wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine napenda kuzungumzia maafa. Sheria Na.7 ya mwaka 2015, Disaster Management Act, imetaja na imefafanua Kamati za Maafa kuanzia ngazi ya Taifa mpaka ngazi ya kijiji. Kwenye ngazi ya Wilaya imemtaja Mkurugenzi kama Mwenyekiti na wajumbe wengine. Leo tuna maafa kwenye kila kona ya nchi hii, ni kwa kiwango gani Halmashauri zina-respond kama hazimuachii Waziri Mkuu pamoja na mama Jenista pale? Ni vyema zikatenga fungu na fungu lile lisibadilishwe likafanye kazi ya maafa. Leo kuna mafuriko kila sehemu kwa hiyo, tunajikuta tunakwepa jukumu letu la msingi tunawaachia watu wengine tunashindwa kutimiza jukumu letu ambalo tunatakiwa tulifanye. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja nyingine ambayo napenda kuchangia ni effective control ya Council, ni vyema Wizara ika control vizuri Halmashauri zake. Naomba nitolee mfano na limezungumzwa hapa ndani suala la Makao Makuu, mfano sisi pale kwetu Mufindi kwa lengo la kupeleka huduma kwa wananchi ilikubalika tuanzishe Halmashauri nyingine lakini Makao Makuu inayojengwa ni kilomita 6 kutoka ilipo Makao Makuu ya Halmashauri ya zamani, hapa ni kwa faida ya nani? Naomba Mheshimiwa Waziri na timu yake ikiwezekana maeneo kama haya wayaundie timu maalum wakayatazame, je, ni kwa maslahi ya wananchi? Hoja siyo wapi ikae lakini inapowekwa Makao Makuu itazame maslahi mapana ya walio wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho siyo kwa umuhimu napenda pia kuongezea kwenye kifungu ambacho kimezungumzwa na wenzangu tukatazame maslahi ya Madiwani wetu, Wenyeviti wetu wa Vijiji na Wajumbe wa Serikali ya Vijiji, hawa ndiyo wanafanya kazi kubwa Zaidi. Hili tunaweza kulifanya kwa namna kuu mbili; moja kama kutakuwa na pesa za Serikali Kuu ziende, lakini pili kuzibana Halmashauri zipeleke kama ni posho au nauli ili wale wanaohangaika na wananchi kimsingi waweze kupata posho kama hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa hotuba nzuri sana ambayo kimsingi jana iliwasilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sehemu kubwa sana ya baadhi ya hoja ambazo nilitaka kuzizungumza nadhani zimekuwa coverd, kwa hiyo ninawashukuru sana. Lakini ninaomba nizungumzie maeneo machache, la kwanza jana hapa amezungumza Waziri wetu wa TAMISEMI na ameonesha jinsi ambavyo atakwenda kuweka msukumo mkubwa kwenye watumishi waliopo kwenye kada ya TAMISEMI. Lakini nilitaka niongezee na nisisitize eneo moja, niwaombe Waheshimiwa Mawaziri kwenda kutazama vyema mazingira ya ufanyaji kazi ya watumishi ambapo wapo kimsingi kwenye Utumishi na TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kupitia ule Waraka wa Elimu Bure sote tulishuhudia jinsi ambavyo tulitoa posho ya madaraka kwa Wakuu wa Shule pamoja na Waratibu wa Elimu Kata, lakini sasa hoja yangu ni nini, niwaomba mkatazame vizuri sana kuhusu watendaji wa kata kwenye nchi hii. Watendaji wa Kata, Maafisa Tarafa hata kwenye vijiji wao ndio viongozi kwenye maeneo yao, Watendaji wa Kata ndio Wakurugenzi kwenye maeneo yao, tumefanya kazi nzuri ya kuwawekea mazingira mazuri ya kazi wenzetu wa elimu na tunao mpango Maafisa wengine wa Ugani lakini bosi ambaye ni Mtendaji wa Kata ana hali gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yeye ndiye anayesimamia madarasa, yeye ndiye anayepeleka taarifa za Kata kwa Mkurugenzi yeye ndiye anayekwenda kusimamia usafi huko, kimsingi hawa ndio wanaofanya kazi kubwa zaidi ya kumwakilisha Mkurugenzi kwenye maeneo yao. (Makofi)

Kwa hiyo hilo ningeomba pia liende sambamba na upande wa Maafisa Tarafa, kada hii huko nyuma kama alivyozungumza mchangiaji mmoja juzi ni kada ambayo kimsingi miongoni mwao ndio tunateua Ma-DAS, tumeteua ma-DED na Ma-DC, lakini changamoto kubwa ipo kuanzia kwenye usafiri ofisi mpaka incentive zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zamani Maafisa Tarafa walikuwa wanapata mishahara ya kiuongozi, baadaye ikaondolewa, ninaishauri sana ikiwezekana tutazame package maalum, maana hawa ndio wawakilishi wa Mkuu wa Wilaya kwenye maeneo yao. Vivyo hivyo kwa ma-DAS katika ofisi zao, utakuta DAS ni kiongozi mkubwa baada ya DC akitoka DAS wanasema anakuja DED, lakini kwa mujibu wa package yake unaambiwa anastahili kupewa gari aina saloon, ni vyema tukahuisha mambo kama haya yaendane sambamba na wakati uliopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia yapo mambo madogo ninayotaka kuyazungumzia, moja; kuna kitu kinaitwa kupanda cheo kwa mserereko, huko nyuma ilikuwepo, hii ni changamoto kubwa watumishi wetu wanayo sasa hivi. Utakuwa mtumishi alikuwa na haki ya kupanda cheo mwaka 2012 hakupanda, alikuwa na haki ya kupanda cheo mwaka 2016 hakupanda, pengine mwaka 2019 hakupanda, sasa anatakiwa apande cheo leo. Na pengine kutokupanda kwake cheo kipindi cha nyuma si makosa yake ni makosa ya mwajiri wake. (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, tuna m-punish yule mtumishi tumeweka mfumo mzuri kwamba kimsingi yule Afisa Utumishi au mwajiri ambaye hakufanya vile atachukuliwa hatua; je, stahiki ya mtu huyu, kwa hiyo niwaomba wenzetu wa Wizara sasa, wakalitazame jambo hili ni watumishi wangapi walistahili kupanda cheo lini kwa haki na kisha waweze kupatiwa stahiki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni recategorization hii ni kubadilishwa kada hapa kuna changamoto na kilio kikubwa sana kwa watumishi wetu, utakuta mtumishi amesoma, ni mwalimu diploma akaanza kupanda cheo labda TGS C akapanda D akapanda hadi E baadaye amefika mshahara wa shilingi 1,200,000; sasa ameenda kusoma degree nyingine ya Utawala au yoyote ile, wakati wa kumbadilisha cheo kutoka kwenye yale aliyoyasomea mambo ya ualimu kwenda huku kwenye utawala ambapo kimsingi mwajiri ameridhia kuna nafasi tunaanza kumpeleka akaanze kupata mshahara kwenye Utawala pale inapoanzia entry point yaani kwa mfano kama HR anatakiwa kuanza kulipwa labda HR II shilingi 700,000 huyu mtumishi alifikia level ya ualimu ya kulipwa shilingi 1,200,000 anarudishwa kwenye HR II, ushauri wangu ni nini, tunaweza either ku-maintain ile personal salary au tukai-quit mshahara wa kule anapotoka vis-a-vis huko anakokwenda ili tusiwavunje moyo hawa watumishi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nililokuwa nataka kulizungumzia pia kwa kidogo ni issue ya madai mbalimbali, kwa mfano nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri aende akatazame madai ya wakufunzi wa Vyuo na Udhibiti Ubora, yako malalamiko ya watu ambao hawakupewa stahiki zao kwa zaidi ya pengine kuanzia mwaka 2018 kurudi nyuma, changamoto ni nini, wanastahili kitu gani? Kama wanastahili wapewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ningependa kuzungumzia kidogo kuhusiana na makundi maalum kwenye utumishi ambao kimsingi Wizara naomba ikasaidie kusimamia, hapa nazungumzia walimu, hapa nazungumzia ma-nurse, hapa nazungumzia madereva, yaani zile kada madereva, walinzi na wale wengine zile kada za chini kwenye level za Halmashauri wale wakubwa wanapata perdiem, wanapata overtime, wanapata extra duty, wengine hawa anaweza kukaa kwenye utumishi wa umma, akafika hata miaka 10 hajawahi kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa mara nyingine kwa kunipa fursa ya kuzungumza katika sekta yetu hii muhimu sana ya maji. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Katibu Mkuu wake pamoja na wataalam wengine, hususan wa pale kwetu Mufindi na katika Mkoa wetu wa Iringa kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru pia Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kwa hotuba yake aliyoitoa alipokuja hapa Bungeni. Kwenye ukurasa wa 29 alizungumzia vizuri sana sekta ya maji. Moja ya changamoto alizozizungumza ni usimamizi thabiti kwa lengo la kufikia malengo yaliyowekwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napongeza, lakini pili, napenda kushauri kwenye baadhi ya maeneo. Pale kwangu nikiri kabisa Mheshimiwa Waziri ameanza kwa speed kubwa na nzuri sana. Unaona miradi kichefu chefu ambayo ilikuwa kero kwa muda mrefu, inaanza kufanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza mchango wangu kwenye eneo langu la Mufundi Kusini, Jimbo ambalo limejitolea kutunza vyanzo vya maji kwa kupanda miti mingi ili Watanzania kwa ujumla waendelee kunufaika na mvua na hatimaye maji tuendelee kuyapata kwa wingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza na mradi wa Sawala. Nakuomba Mheshimiwa Naibu Waziri, umekwenda pale; huu ni mradi wa muda mrefu sana na kuna miradi kama mitatu ambayo imeanzishwa kwa muda mrefu lakini bado haijakamilika japo speed yake kwa sasa inaridhisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nina maombi mawili; moja, napenda kupata commitment yako Mheshimiwa Waziri, utusaidie ili ikamilike haraka iwezekanavyo, ikiwezekana mwaka huu hii miradi iishe. Pili, mradi huu ulikuwa katika vijiji vine; una Vijiji vya Lufuna, Sawala, Mtwango na Kibao. Katika Kata hiyo kuna Kijiji kinaitwa Mpanga na Kitilu, haufiki. Namwomba Mheshimiwa Waziri kupitia atusaidie mradi huu ufike maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tunao Mradi wa Kimilinzowo, nao huu ni sehemu ya miradi kichefuchefu; kwa miaka mingi huko nyuma tangu ulipoanzishwa haukukamilika. Nimeona kasi yako na wataalam, na nimemwona Meneja wa Maji wa Mkoa na Meneja wa RUWASA wa Wilaya wanavyohangaika. Mheshimiwa Waziri toa timeframe, mwaka huu mradi huu ukamilike tumalize kabisa hii kazi. Pia na vijiji Jirani kama Ihawaga vipate maji, Kinegembasi kipate maji, Nyigo napo unasuasua; tusaidie Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, namba tatu, tuna mradi wa Nyororo. Bahati nzuri miradi hii yote Waziri wetu sio mgeni, amefika. Huu mradi wa Nyororo ni mradi ambao unagusa watu wengi kama miradi mingine nilivyoizungumzia, na uko barabarani pale. Changamoto ya mradi huu pia katika Kata yenye vijiji vinne unazungumzia kijiji kimoja. Moja, haujakamilika; naomba pia miradi hii mitatu hebu ikamilike basi. Hii story ya kuzungumziwa mradi umeanza, umeanza, iishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nampongeza Mheshimiwa Waziri, tulizungumza hapa kwenye simu, akazungumza na Katibu Mkuu wake wa Wizara ya Maji, akazungumza na wataalam, wamekwenda site, Meneja wake wa Mkoa na Wilaya wamekwenda kwenye vijiji vingine ambavyo viko katika Kata hiyo; wamekwenda Njojo, wamekwenda Ving’ulo na Nyororo shuleni kufanya design ili iwe extended katika Kata nzima. Nakupongeza sana, lakini wakaenda mpaka na jirani ya Maduma na vijiji vyake vya Honga Maganga, Maduma na Ihanganatwa. Lengo ni kwamba Kata hizi mbili zinufaike na mradi huu. Naomba sana, hebu ukamilike basi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kuzungumzia mradi maarufu kwenye Jimbo letu wa IMAI. Huu ni mradi unaogusa Kata tatu za Ihowanza, Malangali na Idunda. Ni mradi wa muda mrefu sana. Changamoto ni moja tu; miundombinu imechakaa. Nashukuru kuona kwamba katika mwaka huu wa fedha mmezungumza kwamba mtatutengea fedha kwa ajili ya kuufanyia marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana, mradi huu, moja, angalau na wenyewe ukikamilika vijiji zaidi ya kumi vitanufaika. Pili, kama mkianza kuufanyia matengenezo ya miundombinu iliyochakaa, naomba sana Mheshimiwa Waziri aende ukaguse mpaka Kata ya Mbala Maziwa ambako changamoto ya maji ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo ningependa kukugusia miradi mipya. Hapa nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa jinsi alivyoiitikia kwenda kusaidia kuanzisha miradi mipya mitatu katika Jimbo letu la Mufindi Kusini Mungu akubariki sana. Wanamufindi Kusini wanamshukuru kwa jinsi alivyoanza design katika Kata ya Igowole mradi wa kupampu maji ambao utagusa Vijiji vya Ibatu, Nzivi, Igowole mpaka Kisasa. Nimwombe sana, kwanza ni hatua ya kwanza kumaliza jambo linguine, ikianza itimie ndani ya muda mfupi ili wananchi waweze kupata maji katika jimbo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Mheshimiwa Waziri, nimeona ameweka Mradi wa Gravity hapa wa Mgogoro ambao unakwenda mpaka Kata ya Kihohela. Nimshukuru sana kwa sababu eneo hili ndiyo kila siku naongea na Waziri wetu wa Ujenzi hapa, ni eneo ambalo kuna viwanda vingi, barabara ni mbovu, maji ni changamoto, lakini Mheshimiwa Waziri wa Maji, umekuwa msikivu, nakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ombi langu, Vijiji vingine kama Kitasengwa sijaviona, nimwombe aende Kitasengwa, Lole, Lugema mpaka Mabaoni pamoja na Makungu ili wote wanufaike. La pili, Mheshimiwa Waziri anapokwenda kwenye Kata ile ya Kihohela ambayo ni sehemu ya jirani atusaidie, sijaiona Magunguri kwa sababu bado mradi wake haujakaa vizuri, Magunguri na Isaula pia inufaike.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, lakini kabla sijamaliza, nizungumzie kidogo Mradi wa Idete, Kata ambayo ipo kama kisiwani, imeachwa kwa mara ya kwanza wanakwenda kuweka historia ya Mheshimiwa Waziri wetu, maji hayakuwahi kufika pale. Waziri amepeleka visima, nimwombe vile visima alivyopeleka pia apeleke na mabomba ya usambazaji maji ili wananchi wa Idete waendelee kumshukuru Rais wao kwa jinsi alivyomtuma na yeye ameelewa na wasaidizi wake wameelewa, sasa wanakwenda kuwapelekea maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijamaliza nina maombi madogo mawili, madogo tu na nita-mention kwa sababu ya muda wako, najua wachangiaji ni wengi katika sekta hii. Moja, tunayo changamoto kwenye miradi iliyokuwa imeanza kwenye Kata za Kasanga, lakini pia kuna Kata ya Mtambula na vijiji vyake, pamoja na Kata ya Mninga na Luhunga. Nimwombe sana Waziri akajaribu kutazama maeneo haya pia. Namwomba Mheshimiwa Waziri apeleke wataalam pale wakatusaidie ku-design ili kero ya maji iishe. Mto Ruaha unaanzia pale, wao ndiyo wanatunza kwa nini wawe na shida ya maji? Halafu watu wengine wanufaike na maji hawa si ni Watanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia sasa, nipende pia kuwaombea wenzangu wa jirani kwa sababu mradi huu kwa muda mrefu umezungumzwa, mradi wa vijiji 14 ambao unagusa Kata ya Iswagi, Ihalimba na Ikongosi, namwomba sana Wazri ukakamilike mradi huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa fursa hii ambayo umenipatia. Nitaongea kwa kifupi na mambo machache; ukiacha kupongeza kazi kubwa inayofanywa na Wizara hii mpya pamoja na wataalam, lakini niongee kwenye angle mbili tu. Angle ya kwanza, mara kadhaa nimezungumza na Mheshimiwa Waziri pamoja na Mkurugenzi wa Mfuko wa Mawasiliano juu ya changamoto kubwa sana ya mawasiliano kwenye eneo letu la Mufindi Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati fulani waliwahi kuniahidi kwamba wangeleta hiyo minara, niwaombe tu sasa wafanye utekelezaji. Tunayo changamoto kubwa sana kwenye Kata ya Idete ambako wananchi wanabidi wapande kwenye miti ndiyo afanye mawasiliano. Kwa mfano, ukiende pale Idete, utakuta kuna sehemu maalum kama center, zimewekwa Kamba pale kuna mtu anakodisha unapeleka simu yako pale halafu unaweka ukimaliza kuzungumza unarudi nyumbani. Hii si sawa kwa nchi ya level ya maendeleo ambayo tumefikia mpaka sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niwaombe wenzetu, walishaanza kufanyia kazi tayari pale lakini ziko kata jirani ambazo zina changamoto kubwa especially Kata ya Maduma, Idunda, Makungu, Kiyowela pamoja na maeneo mengine machache ambayo yameainishwa. Kwa hiyo niwaombe sana Mheshimiwa Waziri na timu yake watusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nataka pia kutazama eneo moja. Tuna mfumo mzuri ambao tumeuanzisha sasa hivi especially kwa kuanzisha masomo ya computer mashuleni. Hata hivyo, naishauri Wizara wakae chini, watafakari ni namna gani tunaweza kuwafanya vijana wetu wakawa competent. Mambo mawili; moja masomo yale wanayosoma yawe na uhalisia, yawe ya kivitendo zaidi. Wapo vijana wanamaliza mpaka Vyuo Vikuu lakini pengine hata kutengeneza simu hawezi wa masomo ya IT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni changamoto kubwa sana. Hivyo, niwaombe waitazame vizuri mitaala yetu, ni namna gani vijana wanaosoma pengine wako Vyuo Vikuu kama ni ma-IT kama ni ma-engineer wapo kwenye mifumo ya habari, namna gani sasa wakimaliza wanaweza kuja kusaidia huku mtaani ambako kuna changamoto kubwa sana kwenye eneo hili. Kila kitu tunasema sasa hivi kinakwenda kiteknolojia na vijana wako mtaani hawana kazi, kwa hiyo ni changamoto kubwa sana. Namba mbili, tutazame namna ya kutengeneza centers kama hubs, baadhi ya nchi zilizoendelea waliandaa technological hubs kama zamani tulivyokuwa tunafanya maktaba. Unakwenda pale Dodoma Mjini kuna maktaba, vijana wanakwenda pale wanasoma, wanajifunza na kadhalika. Tunaweza kufanya hivyo hivyo kwa maeneo yetu kwenye level ya halmashauri, vijana walio mashuleni na wasio mashuleni wenye uelewa na uelewa mdogo, wakawa wanakutana inasaidia ku-exchange yale mawazo na ku- develop pengine mifumo mbalimbali ya ki-computer, matokeo yake tukaongeza confidence kubwa kwa vijana wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nilitaka tu niongee mambo hayo mafupi. Naunga mkono hoja. (Makofi)

Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuanzia Januari, 2021 hadi Februari, 2022 pamoja na Taarifa ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kwa Kipindi cha Januari 2021 hadi Januari 2022
MHE. DAVID M. KIHENZILE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi hii ili niweze kuhitimisha hoja ya Kamati yangu, lakini na mimi niungane na Wabunge wenzangu kukupongeza kwa ushindi mkubwa ulioupata kwa nafasi ya Naibu Spika wetu. (Makofi)

Niwapongeze na kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge waliopata nafasi ya kuchangia kwenye hoja yangu, kwa uchache Mheshimiwa Cecil Mwambe, Engineer Ezra Chewelesa, Mheshimiwa Maryam Omar Said, Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mheshimiwa Juma Usonge, Mheshimiwa Humphrey Polepole, Mheshimiwa Neema Lugangira, Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mheshimiwa Exaud Kigahe, Mbunge na Naibu Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara na Mheshimiwa Dkt. Suleiman Jafo, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja mbalimbali zimezungumzwa katika kuchangia kwenye hoja zetu, lakini pamoja mambo mengine kwa kirefu sana imezungumziwa hoja ya Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hoja zingine tunaamini Serikali imechukua na kwa uzito mkubwa itakwenda kufanyia kazi hoja hizo kwa maslahi makubwa ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba Bunge lako Tukufu sasa lipokee na kukubali maoni ya Kamati yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa hoja.

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, naafiki.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DAVID M. KIHENZILE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA VIWANDA, BIASHARA NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru Waheshimiwa Wabunge waliochangia hoja mbali za kamati yetu lakini ikiwa ni pamoja nakuunga mkono maazimio yetu. Sitaenda kwa mtu mmoja mmoja lakini waliochangia karibu wajumbe 10 ambao wametoa maoni mbalimbali. Cha kwanza nishukuru Serikali kupitia mawaziri kwa kukubali kufanyia kazi hoja zetu ambazo tumezitoa, kuanzia Mheshimiwa Waziri wa Mazingira Mheshimiwa Jafo, lakini pia na Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara Mheshimiwa Ashatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hoja zake kuu za mwishoni ikiwa ni pamoja na kutoa commitment ya Serikali kulipa bilioni 15 kama fidia kwa wananchi waliopo kule Ludewa kwenye mradi huu wa Liganga na Mchuchuma. Vilevile kutoa kauli ya Serikali juu ya majina mabaya yanayopewa wafanyabiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nataka niseme kidogo kama tuko serious kama Taifa tunahitaji kuvutia uwekezaji nchini, tujue tuna kazi kubwa sana ya kuvutia watu waje kuwekeza kwenye nchi yetu wasiende kwenye nchi nyingine. Kuwambia wafanyabiashara wenye option ya kwenda kwenye nchi hii au nchi nyingine ni wezi, ni mafisadi ni kuwa-discourage. Matokeo yake hawatokuja kwetu, watakwenda kwenye nchi nyingine halafu tutabaki tunaulizana hapa kwa nini nchi yetu katika wafanyaji biashara ni ya141 kati ya nchi 190. Kwa hiyo, nimshukuru Mheshimiwa Waziri na tuone utekelezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hoja nyingine ambayo kidogo niifafanue ya Liganga na Mchuchuma. Sote ni mashahidi Liganga na Mchuchuma Makaa ya Mawe yaligundulika mwaka 1860 wakati Liganga mwaka 1898 ukipiga hesabu kwa mfano Makaa ya Mawe tangu yagundulike mpaka leo ni miaka 185 tunaendelea bado kufanya jitihada. Umuhimu wa Liganga na mchuchuma kwa maslahi ya watanzania hauyumkuniki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano makaa ya mawe yana deposit ya tani Milioni 428 ambapo tukianza mradi huu kama case study tutapata makaa ya mawe karibu Milioni tatu kila mwaka. Pili, moja ya changamoto kubwa ambayo taifa letu linapata kwa sasa ni kuagiza chuma kutoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninazo takwimu kwa miaka mitano peke yake Taifa la Tanzania limetumia takribani trilioni tano kuagiza chuma kutoka nje. Fedha hizo zimeagizwa kwa njia ya USD dolla za kimarekani. Kwa mfano mwaka 2018, takribani dola 400,100/= tulitumia kuagiza chuma, 2019, 1.1 trilioni. Ukiangalia mapato hayo ni takribani sawa na fedha ambazo tunazikusanya za TRA kwa mwaka kwa miaka hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa mradi huu hauyumkiniki, ukija kwa mfano kwenye aspect namba tatu, tulisema mradi huu ukikamilika utasaidia kujenga barabara za lami kutoka Njombe mpaka kwenye eneo la mradi kwa zaidi ya kilomita 221. Tutajenga reli, tutajenga bandari lakini kama haitioshi tutaingiza kwenye gridi ya Taifa Megawatt 600. Sisi Kamati ya Viwanfda na Biashara tumefanya ziara kwenye viwanda, tumekuta baadhi ya viwanda wanalalamika umeme umekatika Zaidi ya mara 20 kwa mwezi mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni Megawatt nyingi tulielezwa kati ya Megawatt 600, takribani Megawatt 250 ingetumika kwenda kuchakata chuma, 350 ingeingizwa kwenye gridi ya Taifa. Kutoka mwaka 2015 mpaka 2020 tumeongeza takribani Megawatt 300 kutoka 1300 mpaka 1600. Hivyo umuhimu wa jambo hili hauna mjadala. Hata hivyo kama kamati tunaendelea kusimamia lazima tuweke maslahi ya Taifa mbele. Haiwezekani, haikubaliki na haiwezi kuvumiliwa na watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anakuja na dolla Millioni 600 anatumia dhamana za Taifa letu 2.4 bilioni halafu anapata mgao wa 80 percent ninyi mnapata asilimia 20. Hii biashara haiwezi kuwepo. Sisi kama kamati hatukubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama kamati haikubaliani, hii ni sawa na mikataba ya zamani ya akina Mangungu wa Msovero. Ndio maana tunaungana na Serikali walipoamua kufanya review upya, kupitia terms, kupitia vivutio kipi kilikubalika. Kama tulikubaliana kwenye awamu ya kwanza tulikosea kwa hiyo, twende kwenye awamu ya pili tukubali? Haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunaiunga mkono Serikali, hata hivyo mambo mawili au matatu kaa tulivyo andika kwenye ripoti yetu: -

(i) Uharakishwaji ufanywe kwenye mjadala huo. Aidha kwa mkandarasi huyo au mwingine ili wananchi wa Taifa hili waache kuagiza chuma kutoka nje, wananchi wa Taifa hili wapate umeme tunaouhitaji, taifa hili tujengewe lami, ile southern corridor iweze kuwa improved;

(ii) Fidia, wale wananchi wasio na hatia ambao hawahusiki hata kwenye mijadala yetu ni vema walipwe fidia yao mara moja. Tunaipongeza Serikali kwa mambo mawili; moja, kwa kufanya review kwa sababu uthamini wa kwanza ulikuwa unaonesha bilioni 13, lakini wakasema tukiwalipa thirteen billion itakuwa ni kuwaonea kwa mujibu wa Sheria. Wamefanya review na sasa imeonekana ni bilioni 15 tunaiomba Serikali illipe mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo na kwa sababu na mengine nimeshazungumza kwa umoja wake pamoja na ushauri ambao umetolewa na Wabunge mblimbali naomba sasa kutoa hoja.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa fursa ya kunipa nichangie wizara hii, kwa sababu pia ni wizara yangu ya kwanza kuchangia. Moja nitumie nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, kwa hotuba yake nzuri lakini pia aina ya uwasilishaji ambao unavutia. Sisi sote tunafahamu kwenye maji yako mambo manne la kwanza tunajadili rasilimali, la pilli tunajadili uwezo wa kusambaza maji hayo, la tatu tunajadili hali ya maji taka na la nne tunajadili ubora wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kabla sijaanza huko, nitumie nafasi hii kumpongeza Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. Amefanya mapinduzi makubwa kwenye sekta hii ya maji na hapa imeelezwa mambo aliyoyafanya sitoweza kusoma moja moja. Lakini amekamilisha miradi 1373, amekamilisha miradi kwenye miji 80 inayokwenda kuhudumia watu 4,000,000 lakini zaidi ya yote ametusaidia miradi vichefuchefu ikiwemo kule kwangu Sawala Mufindi Miradi 157 kati ya 177, Mheshimiwa Waziri hongera sana kwa usimamizi wa jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeona mchakato wa miradi Miji 28 ambayo na Mafinga, Makao Makuu ya Wilaya yetu ya Mufindi kwa Ndugu yangu Chumi unakwenda kuanza, hongereni sana Wizara. Lakini pia tumeona asilimia imefika asilimia 77 kwenye maji vijijini ambapo kimsingi ndiko ninakotoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma ripoti water utility performance review report for the financial year ya mwaka 2021/2022 imejielekeza katika mambo mbalimbali kwa kina yameainishwa mle ndani. Naomba nisome kakipande kadogo sana anaesema during financial year... nitaitafsiri katika Mwaka huu wa fedha wa 2021/2022 uzalishaji wa maji uliongezeka kwa asilimia 1.2 lakini in stored water production capacity uwezo ulikwenda mpaka asilimia 2.6 lakini upande wa pili mahitaji ya maji yaliongezeka mpaka kufika asilimia 9.8 kulinganisha na mwaka uliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ndipo hoja zangu mbili zinapokwenda kuibuka.tunafahamu Taifa letu, tuna fursa nyingi ambazo tunazo na pengine kabla sikufika huko nimalizie kushukuru kwenye upande wa Jimbo langu. Mheshimiwa Waziri, sina deni na wewe nakushukuru sana wewe, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, watendaji hususani wa kinamama wale viongozi wangu meneja kwenye wilaya na mkoa kwa kazi kubwa ambayo mmenifanyia katika mwaka uliopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yote niliyotamani kusema leo nitegemee niongee kwa bashasha nije na takwimu umenifilisi. Ninachokuombe kheri, naomba ukaitekeleze ikafanyike kwa ufanisi mwaka jana ulianza Mradi wa Igowole nilikuomba ufanye extension isiishie Mkalala, Ikwega na Igowole nimeona hapa unapeleka mpaka Itulituli, Kihanga, Mninga, Kisasa, Kidatu, Uvizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilieleza juu ya umuhimu wa Kata ya Mtambula nimeona umeiweka humu ndani kwenye maji mwaka huu. Nimezungumza kuhusu mradi wa vijiji vya Sambalamaziwa nimeviona humu ndani, japo sijaona Iramba na Kindegebasi nitaomba utuongezee hapo pamoja na Namkangu kule Idunda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa Malangali niliulizia sana mwaka jana leo Mheshimiwa Tendaga amezungumzia, nimeoa amuweka hapa leo pia, mradi wa Itika – Horo na Idete nimeona pia umeukumbuka. Kwa ujumla maeneo karibu yote ambayo tulikubaliana umeyaweka kwa hiyo, kama mchangiaji wa kwanza pia sishiki shilingi yako, nakuombea kheri ukatekeleze Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu kwako na Wizara yako, kuna changamoto kubwa sana na uchelewaji wa kuanza kwa miradi. Sisi Mikoa yetu mitatu tulikuwa na afisa manunuzi mmoja haiwezekani vijana wako wengi mtaani hawani kazi kwa nini mtu mmoja apewe jukumu la miradi yote hiyo? Lazima mkarekebishe hili mwaka wa fedha unaofuatia Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili kwa Mheshimiwa Waziri ni moja tu ni uanzishwaji wa Gridi ya Taifa ya Maji. Kabla sijasema hiyo nikuombe nendeni mkarekebishe Sera ya Maji ya 2002 imepitwa na wakati. Hatuwezi kutumia sera ya miaka 10 iliyopita, miaka 20 iliyopita wakati muda umepita ebu karekebisheni, tusaidieni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye hoja dhidi ya maji ya Taifa, Taifa letu lina bahati kubwa sana hapa umetuambia mvua zinanyesha kwa wastani milimita 1,000 kwenda mbele, hapa tumeelezwa tuna maji ya bahari, tuna Ziwa Victoria, tuna Tanganyika, tuna Nyasa. Katika Ziwa Victoria sisi kama moja ya watu wenye majority shares zaidi ya utilization kubwa inafanywa na wenzetu wa Kenya sisi tupo tunaangali. Mikoa jirani tunaambiwa hapa jana kwamba ina changamoto ya ukame na itakosa chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tanganyika sisi tuna majority share kwenye ziwa lile lakini tunao mradi mmoja tu maji nenda Nyasa maji yake yanafaa kwa kunywewa na mwanadamu hakuna mradi hata mmoja, acha maji ya mvua Mheshimiwa Waziri wakati umefika wa kutekeleza kuanzisha gridi ya maji tukusanye maji yote ya nchi hii yaingizwe ndani tuweke ma– pipe makubwa yasambaze maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri nchi yetu katika nchi zenye highest pick Afrika, Tanzania ni moja wapo tunakwama wapi? Umetueleza mahitaji ya maji kwa sasa ni takribani bilioni 60 lita za ujazo, ume–project miaka 20 ijayo 2035 tutakuwa na bilioni 80 na wakati huo capacity ya maji tulizonazo ni 126 bilioni. Je, hayo mahitaji 2035 tutapata wapi maji? lazima twende tukaanzishe gridi ya Taifa ya maji kama ilivyo gridi ya Taifa ya umeme ili tuweze kupata maji ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Bashe jana amekuja hapa na hoja ya irrigation, gridi ya Taifa ndiyo mkombo. Tutapata maji kwenye viwanda, tutapata maji ya kilimo, tutapata maji kwenye uvuvi, maji ya wanyama pori, maji ya kunywa na kadhalika Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo katika mambo takayoyazungumza ambayo nategemea mwisho wa siku…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa, Ahsante Kengele ya pili.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa uliyonipatia ya kuweza kuchangia na kwa sababu ya muda nitajitahidi niende kwa haraka haraka. Moja, ni kutoa pongezi kwa kazi kubwa ambayo inafanyika na Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye kule Mufindi tuna msemo wetu kwamba, mfupa ulioshindikana, Samia anautafuna, kwa sababu mambo mengi yaliyoshindikana yameanza kufanyiwa kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nashukuru hotuba nzuri sana ya Waziri wa Fedha. Kimsingi ni hotuba nzuri inayotoa uelekeo wa Taifa letu na tuna imani kubwa sana na Wizara kwa namna mnavyomsaidia Rais wetu. Namshukuru sana Katibu Mkuu wa CCM kwa ziara zake kwa sababu kwenye Jimbo letu la Mufindi Kusini ametugusa moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, niungane pia na wengine wanaomwombea Spika wetu heri katika ushindi wa nafasi anayoiomba huko mbeleni kwa sababu amedhihirisha weledi mkubwa katika kuongoza Bunge letu. Tunaamini akiwa Rais wa IPU atafanya vizuri zaidi pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kazi kubwa ambayo imefanya kwenye Mkoa wetu wa Iringa. Tunaona mipango mikubwa ya ujenzi wa uwanja wa ndege, tunaona barabara kubwa za Ruaha National Park na ndugu yangu hapa, jirani yangu wa pale Kilolo, naye barabara yake ya Ipogoro inakwenda vizuri, kwa kweli tunashukuru Mungu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee Mufundi Kusini, Mpango wa EPC + F ambao umeweza kufanyika umesaidia pakubwa sana, unaanza kujenga barabara yetu ya Mafinga kwenda Mgololo na maeneo mengine kama barabara ya Sawala, miradi ya maji ya Mbalamaziwa, Malangali, mradi wa Igowole pamoja na maeneo mengine mpaka kule Mgololo. Pia tunashukuru kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha VETA pamoja na kiwanda kikubwa cha kuchakata parachichi katika eneo letu la Nyororo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maombi machache, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha anisikilize kwenye eneo hili na atusaidie. Rais Mheshimiwa Dkt. Samia amefanya ziara mwaka 2022 mwezi wa Nane, akaahidi barabara ya Mafinga – Mgololo na Nyororo – Mtwango. Tunashukuru kwanza Mafinga – Mgololo imeshaingizwa tayari na mkataba umeshasainiwa; Nyororo – Mtwango pia imeshatajwa kwenye bajeti, lakini imewekewa Shilingi milioni 500 tu, imeleta sintofahamu kubwa kwa wananchi wote. Hata ile furaha waliyokuwanayo kwa Rais wetu imeanza kuwa simanzi. Tunaomba unapoenda kuhitimisha Mheshimiwa Waziri wetu utuambie kuhusu barabara ya Nyororo – Mtwango kilometa 40, tusaidie angalau hata kilometa zianze hata kama zikiwa 20 au 30 ili hatimaye iweze kukamilika barabara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ombi letu lingine kubwa ni kwamba tunataka wenzetu wa Wizara ya Mifugo watusaidie vifaranga angalau milioni tano kwenye mabwawa yetu, wakati huo wenzetu wa Wizara ya Maji tunaomba mtusaidie kumalizia ujenzi wa Bwawa la Iramba pamoja na Ihuwanza. Ninaamini Mheshimiwa Aweso yuko pale atakamilisha hoja hii na ataweza kutusaidia iwe kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wa TAMISEMI, Jimbo la Mufindi Kusini ndiyo jimbo pekee ambalo halijajengewa kituo cha afya hata kimoja tangu miaka miwili tulipoanza. Tunaomba kituo cha afya cha Mgololo na cha Mtwango mtusaidie. Kama haitoshi, tunaamini na tunaomba kabisa kituo cha afya kwa wenzetu wa Wizara ya Mambo ya Ndani watusaidie pale Nyororo ili tuweze kuimarisha ulinzi na usalama kwenye eneo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu. Moja, kwenye upande wa mapato, tunalo eneo muhimu sana, hapa tunazungumzia kuhusu mapato. Nataka Serikali itujengee mambo yote haya. Yako maeneo ya kupata fedha mojawapo ni eneo la biashara ya carbon. Wenzetu wa Gabon tumeambiwa watapata shilingi milioni 150, wenzetu wa Ghana wana pato la shilingi milioni 4.9, Ndugu yangu Kakoso kule kwake ana vijiji nane tu, kapata shilingi bilioni nne. Sisi tuna vijiji 12,000 hivi hatuoni kama kuna mabilioni ya pesa hapa? Hebu tutazame Wizara ya Fedha tukatafute pesa hapa, tukafanye kazi ya wananchi na kusaidia Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, naomba mtusaidie kwenye kuboresha biashara nchini. Tunahitaji kuongeza walipakodi kama ambavyo kwenye hotuba wamesema, tax base iongezeke, lakini mkakati wa kuwajali na kuwaheshimu walipakodi kwa kweli hauridhishi. Tunawaomba Wizara ya Fedha mtusaidie, acheni utaratibu wa kukimbilia kufungia watu maduka. Wale ni Watanzania wenzetu, kaeni nao chini, zungumzeni nao, wapeni ushauri, wafundisheni. Hamkupelekwa shule ili kwenda kuzalilisha na kunyanyasa wafanyabiashara wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hoja hiyo pia nigusie kidogo kwenye ajenda ya upande wa Wizara ya Kilimo. Wenzetu wa Wizara ya Kilimo wana ajenda ya twenty thirty ni hoja ambayo ukiisikiliza inabeba maono makubwa. Wana mpango ikifika 2030 tuweze kupata tupunguze umasikini kwa takribani 64%. Tutakuwa tumefanya kazi kubwa lakini tunahitaji 17.3 trillion. Naiomba Serikali ianze kutenga fedha kila mwaka ili hatimaye tuweze kuja kufikia hatua ya kuweza kuboresha na kufanya mapinduzi makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu na tunatambua kwamba tayari tumeshaongeza Bajeti ya Kilimo kutoka shilingi bilioni 294 mwaka juzi, mwaka jana ikafika shilingi bilioni 754, mwaka huu shilingi bilioni 970 lakini twende zaidi tufanye kilimo, mifugo na uvuvi kama ajenda namba moja kama tulivyofanya miundombinu kwa miaka mitano mpaka saba iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo hayo nipende kushukuru sana kwa kunipa fursa hii ahsante sana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kuwasilisha kwako maombi ya Wanamufindi kukuomba upatikanaji minara kwenye maeneo yenye kero kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kuomba minara ya simu maeneo yafuatayo; Kata ya Maduma, Kata ya Kasanga Makao Makuu ya Kata, Kata ya Kiyowela, Kata ya Makungu sehemu za Kitasengwa, Kata ya Igowole sehemu za Kisasa na Ibatu na Kata ya Nyololo katika baadhi ya sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna maombi ya kompyuta ili kuunga mkono sera yetu ya Make Mufindi Digital. Niombe kompyuta 500 kwa ajili ya shule 10 za kuanzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kushukuru Serikali kipekee kiongozi Mkuu wa Serikali ambaye ni Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Ninamshukuru kwa sababu mbili; sababu ya kwanza ni kwa sababu ya wataalam ambao amewapa kazi ambao ni Waziri wetu wa Ujenzi, Naibu Mawaziri, pamoja na watendaji wake.

Mheshimiwa Spika, lakini namshukuru kwa sababu ni kiongozi ambaye anaamini kwenye maono pamoja na matokeo. Nimetumwa na watu wa Mufindi Kusini leo kama barabara za Nyololo - Mtwango na Mafinga - Mgololo hazipo kwenye bajeti nigomee kupitisha bajeti hii leo. Kwa sababu wameahidiwa kwenye Ilani ya CCM, msururu wa viongozi wamefika huko, lakini pia unyeti wa maeneo hayo, lakini nafikiri msimamo wangu nilioingia nao utakuwa mlegevu kidogo. Kwa mara ya kwanza watu wa Mufindi Kusini tumeona kwenye bajeti ukurasa 173 ujenzi wa barabara ya kutoka Mafinga - Mgololo kilometa 78, na ujenzi wa barabara Nyololo - Mtwango kilometa 40.

Mheshimiwa Spika, ukiacha kwamba kwenye Ilani ya CCM yamesemwa nikikueleza orodha ya viongozi waliotembelea Mufindi Kusini, nikikueleza unyeti wa maeneo hayo, kwa maana ya viwanda unaweza ukasikitika sana. Wote tunafahamu kwamba Mufindi Kusini makampuni makubwa ya chai yote nchini Tanzania yako Mkoa wa Iringa, yako Mufindi, yako Mufindi Kusini. Kiwanda kikubwa cha karatasi Barani Afrika na ukanda wa Afrika Mashariki cha Mgololo kiko Tanzania, kipo Mkoani Iringa, kipo Mufindi Kusini.

Mheshimiwa Spika, viwanda vya nguzo kwa wingi katika nchi yetu viko Iringa, viko Mufindi Kusini. Siyo hilo tu hata shamba kubwa la miti katika nchi yetu la Sao Hill liko Mufindi Kusini pamoja na Mafinga. Lakini pia hata viwanda vya fiberboard viko pale Mufindi Kusini nikianza kuvitaja kwa uchache hapa pamoja na faida zake nitataja kimoja tu cha Mgololo.

Mheshimiwa Spika, Kiwanda cha Mgololo kimeanza miaka ya 1980, kina supply karatasi ukanda wote huu, chenyewe peke yake kina magari zaidi ya 70 ma-heavy trucks, lakini yako magari mengine yanayoingiza mizigo pale ndani zaidi ya 90, yako yanayokuja kwa ajili ya kufanya boiler (kuchemsha maji) kwenye kiwanda yako 90, viko viwanda vya Wachina pembezoni. Kwa hiyo kiwanda hiki kinaajira zaidi ya 7,000, magari zaidi ya 200 na kodi yake peke yake ni zaidi ya bilioni pengine 25 mpaka 30. Ukivichanganya viwanda hivi vinaiingizia Serikalini kodi ya zaidi ya bilioni 50 kwa mwaka mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukichukua kwa miaka 10 ni bilioni 500; barabara tunazozitaji kuzijenga hazihitaji hata bilioni 120 watu wa Mufindi wanauliza wamemkosea Mungu nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikikupa orodha ya ziara ya viongozi kuanzia mwaka 1980 nimechukua sample tu; tarehe 10 Oktoba Mwalimu Nyerere alifika pale Mufindi Kusini; tarehe 10 Aprili, 1987 aliyekuwa Waziri wa Ulinzi Salim Ahmed Salim alifika Mufindi Kusini akaahidi; tarehe 30 Aprili Rais wa Awamu ya Pili Ali Hassan Mwinyi alifika kwenye kiwanda hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kanali Kinana - Waziri wa Ulinzi alifika pia tarehe 12 Juni; lakini Mwalimu Nyerere tena tarehe 4 Agosti, 1988 asubuhi saa tatu alifika tena akitoa ahadi hizo hizo. Wana Mufindi wakiahidiwa hayo hayo. Haikuishia hapo Makamu wa Rais Dkt. Omar Ali Juma yeye alichelewa kidogo alifika saa tano alifika tarehe 9 Machi, 2002. Aidha, Rais wetu wa sasa akiwa Makamu wa Rais alifika Mufindi Kusini katika Kiwanda cha Mgololo tarehe 11 Februari, 2018 akaahidi, haikuishia hapo tarehe 1 Oktoba, 2021 Mheshimiwa Mizengo Pinda alifika; orodha ni ndefu Kasekenya ametumwa na Waziri Mbarawa amefika, Mheshimiwa Waziri Mkuu bahati mbaya hayupo hapa leo alifika Iringa alizungumzia. Dkt. John Pombe Joseph Magufuli tarehe 29 Septemba, 2020 akiomba kura alifika Mufindi Kusini; Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete akiwa Rais mwaka 2005 alifika pale na akazungumza. Wote hawa walikuja na wakaahidi ujenzi wa barabara hizo.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye mpango wa tatu na mpango wa pili wa miaka mitano theme yake kuu ilisema naturing industrialization for economic transformation and human development. Ukiangalia anazungumzia viwanda, anazungumzia kuongeza manpower ya watu.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye Ilani ya CCM, ilani yetu ya CCM ambayo sehemu kubwa tuko hapa ukiangalia kifungu cha pili anasema moja ya majukumu yetu itakuwa ni kukuza uchumi wa kisasa fungamanishi, jumuishi na shindanishi unaojengwa kwenye misingi ya viwanda huduma za kiuchumi na miundombinu wezeshi.

Kwa nini tunapiga kelele kuhusu kujenga barabara ya Mufindi Kusini? Sitaki kusema nchi hii maeneo mengine siyo muhimu sana, lakini tutakuwa ni watu wa ajabu sana dunia itatushangaa unakimbilia kujenga maeneo ambayo hata production iko chini unaacha sehemu ambapo ukiongeza barabara, ukijenga barabara, utasafirisha bidhaa, utaongeza uzalishaji hata dunia itakushangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ombi langu moja nimepongeza viongozi kwa hatua kubwa ya kuingiza kwenye mpango leo na watu wa Mufindi Kusini leo wanashangilia. Lakini tunaomba barabara hizi zianze kujengwa sasa nimezungumza na Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, tumekutana zaidi ya mara 11, zaidi ya mara tisa tumekutana na Naibu Waziri, lakini tumezungumza na Waziri wa Fedha nimefurahi kuona leo wamekubali kwamba barabara ya Mafinga - Mgololo itaanza kujengwa katika utaratibu wa kawaida. Lakini Nyololo - Mtwango itajengwa kwa mfumo wa EPC + unfinanced kwa maana engineering, procurement, construction na finance na amenihakikishia Waziri mwaka huu wa 2022 inaanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, nikuombe wewe kwa nafasi yako pia pamoja na Serikali kwa ujumla ahadi hii ya Serikali na ili tuendelee kuonekana watu serious mbele ya Watanzania ujenzi huu uanze mara moja. Tumepiga danadana kwa miaka 60 sasa hatimaye tukatekeleze na wananchi wetu waone umuhimu wa wao kuelekeza eneo lao kwa ajili ya uchumi wa viwanda na tuzidi kuongeza ajira zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)