Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Janejelly Ntate James (2 total)

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na usumbufu mkubwa katika mafao ya watumishi mara wanapostaafu, kukiambatana na kuchukua muda mrefu. Je, ni nini tamko la Serikali juu ya kuwawezesha hawa wastaafu wetu ambao wamelitumikia Taifa kwa juhudi kupata mafao yao kwa wakati?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la mafao ya wafanyakazi nataka niwahakikishe wafanyakazi tumeendelea kuliratibu ndani ya Serikali kupitia Mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii na wote mnatambua tulikuwa na Mifuko mingi ikaleta usumbufu mkubwa sana. Nini tumekifanya? Tumekusanya Mifuko yote ya Hifadhi tumeunda Mfuko mmoja PSSSF ambao upo chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mfuko huu umeendelea kuratibu kwanza idadi ya wafanyakazi wote waliokuwa wanalipwa na mifuko ile mbalimbali na kuweka utaratibu wa wale waliostaafu ambao walikuwa hawajalipwa kuanza kuwalipa na wale ambao wanastaafu kuendelea kadiri tunavyopata fedha na wale ambao watastaafu siku za karibuni wote wanaratibiwa vizuri ili tuondoe usumbufu uliokuwepo.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba bado kuna wachache hawajapata mafao yao kwa muda, lakini Serikali inaendelea kulipa wastaafu kadri inavyoweza kupata fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, siku za karibuni hapa nilikuwa nazungumza na wafanyakazi wa TALGWU, wa Serikali za Mitaa na hiyo ilikuwa ni moja kati ya jambo ambalo wao walitaka kulijua na mimi niliwahakikishia kwamba Serikali inaendelea na mwezi wa Nne tumelipa zaidi ya bilioni 172 wastaafu na tunaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuwalipa wastaafu. Pia Mfuko huu umerahisisha namna ya wafanyakazi waliostaafu kuufikia; tumefungua Ofisi ya PSSSF kila Mkoa ili wastaafu waweze kufika pale mkoani.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha pia mfumo wa kielekroniki wa mawasiliano kati ya wastaafu na makao makuu. Kwa hiyo, mstaafu huko alipo anaweza kuwasiliana na makao makuu kupata taarifa mbalimbali. Tutaimarisha elimu kwenye hili ili kila anayestaafu aweze kujua na aweze kulipa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, huo ndio mkakati ambao tunaendelea nao, tunajitahidi sana na narudia tena tunatambua kwamba wapo wastaafu ambao bado hawajafikiwa kulipwa fedha zao, lakini nataka niwahakikishie tutawalipa haki yao. Huo ndio msisitizo ambao tumewasisitiza waajiri watunze kumbukumbu za watumishi wao kutoka wanapowaajiri mpaka wanapomaliza ajira zao.

Mheshimiwa Spika, huu Mfuko tumeendelea kuusimamia hata Waziri wa Nchi wiki moja iliyopita amekaa kikao na wale watumishi wa Mfuko ule kwa kujiridhisha kama je mambo yanaenda sawasawa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kulipa mafao tunatambua wengine bado hawajalipwa lakini tutawalipa. Kwa hiyo, naomba nitumie nafasi hii kuwahakikishia wastaafu kwamba kila aliyestaafu atalipwa fedha yake ya mizigo kurudi nyumbani na vile vile ile pensheni ambayo ilipaswa kulipwa wakati wote anapokuwa kwenye ustaafu. Hayo ndio malengo ya Serikali. (Makofi)
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza naipongeza Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa jinsi inavyojitahidi kuboresha elimu nchini, hongereni sana. Nina swali dogo tu, Serikali sasa mtuambie mna mkakati gani wa kuweza kutosheleza walimu wenye weledi kufundisha masomo haya ya amali ukichukulia tuna upungufu wa walimu nchini?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janejelly Ntate, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri kwamba tunao upungufu wa Walimu kwenye shule zetu kwa ngazi mbalimbali na hii inatokana na kuwepo kwa Walimu wanaostaafu, wanaotangulia mbele za haki na wagonjwa ambapo tunajua yapo mapengo ya ufundishaji hasa kwenye eneo hili la elimu ya amali.

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali kwenye mpango huu ni kuhakikisha kwanza, tunaendelea kupokea vibali vya ajira kama ambavyo Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyotoa vibali vya kuajiri walimu, miongoni mwa Walimu ambao tunawaajiri hasa tunaangalia zaidi kwenye eneo hili la elimu ya amali ili kuwezesha utekelezwaji mzuri wa Sera hii mpya inayogusa kwenye maeneo ya amali ili kuwezesha ufundishaji na wanafunzi waweze kupata elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkakati wetu ni kuongeza ajira kwenye sekta ya elimu ili kuwa na walimu wa kutosha, ahsante. (Makofi)