Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Janejelly Ntate James (21 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JANEJELLY J. NTALE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa jicho lako kuniona, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha kuwa mmojawapo wa Bunge la Kumi na Mbili. Lakini niwashukuru wakinamama wa UWT Mkoa wa Dar es Salaam na Baraza Kuu la UWT Taifa na wajumbe wengine wako humu ndani ya Bunge kwa kuniamini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nishukuru Chama cha Mapinduzi kwa sababu ndiyo chama pekee kinatupa nafasi watumishi wa Serikali ndani ya Bunge hili, ahsanteni sana. Lakini nimesoma risala zote mbili, Mheshimiwa Rais anaongelea maboresho ya watumishi na maslahi ya watumishi, tunashukuru sana alivyohamishia Serikali Dodoma ametekeleza kilio cha watumishi wa Serikali na vyama vyao ambavyo tulikuwa kila siku tukishauri hilo, tunamshukuru sana.

Lakini tumshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye alisimamia zoezi hilo aliposema kila mtumishi kuondoka Dar es Salaam ahakikishe akaunti yake imesoma, tunakushukuru sana. Lakini tunampongeza Rais kwa jinsi alivyojenga mji wa Kiserikali Mtumba, mji huo umeleta mahusiano kazini kwa kufanya Wizara kati ya mtumishi na mtumishi kufahamiana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais kwenye risala yake anasema ataboresha maslahi ya watumishi, lakini niombe kushauri ili maslahi ya watumishi yaboreshwe turudi kwanza tuangalie sheria za kiutumishi, kuna baadhi ya sheria yatafanya zoezi hili liwe gumu. Kuna sheria moja inaitwa sheria ya re-categorization…

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Ntale ukae chini upokee taarifa, Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sababu ya muda nitaenda kwa kifupi sana.

Mheshimiwa Ntale ningependa kukupa taarifa kwamba umesema Chama cha Mapinduzi ndiyo cha pekee kutoa fursa kwa watumishi wa umma, ujue kwamba tulikuwa tuna Mbunge anaitwa Dkt. Sware Semesi alikuwa ni Mhadhiri wa Chuo Kikuu, alikuwa ni Mbunge wa CHADEMA, alikuwepo mama Lyimo alikuwa ni Chancellor wa Chuo Kikuu pale alikuwa ni Mbunge wa CHADEMA, mimi peke yangu nilikuwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ni Mbunge, kwa hiyo usipotoshe, na wengine wengi.

SPIKA: Mheshimiwa Janejerry James Ntale unaipokea hiyo taarifa?

MHE. JANEJELLY J. NTALE: Mheshimiwa Spika, naomba nisiipokee hiyo taarifa kwenye Chama cha Mapinduzi kimetenga nafasi mbili kabisa kwamba ni nafasi za watumishi wa Serikali kutoka kwenye vyama vya wafanyakazi na humu ndani tuko wawili mimi na Dkt. Alice, sipokei hiyo taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naongelea sheria ya re- categorization. Sheria hii kama haijaumiza mtumishi yeyote aliyehumu itakuwa imeumiza mtoto wako au mpiga kura, ile sheria mtumishi akijiendeleza, akiomba kufanyiwa re- categorization anashushwa mshahara na kwenda kuanzia kwenye cheo kile cha wale wengine waliopo.

Mheshimiwa Spika, binafsi sisi hatupingi mtu kwenda kuanzia pale wanapoanzia wataalam wale, lakini aachwe na mshahara wake. Kwa sababu nimefanyakazi Wizara ya Fedha kila mtumishi ana budget line yake ya mshahara huyu mtumishi hakuna anapoongeza bajeti, mshahara wake unakuwa ni ule ule, alichobadilisha ni kada, niombe hiyo sheria, Menejimenti ya Utumishi wa Umma mkaiangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Jenista ni shahidi tumekuwa tukikulilia kilio hiki cha sheria hiyo inaumiza sana watumishi. Lakini kuna na miundo ambayo siyo rafiki tena kwa watumishi, leo hii Mheshimiwa Rais tunamshukuru ameunda Wizara ya TEHAMA.

Lakini kwenye muundo wa ma-executive assistant ambao ndiyo wasaidizi wenu bado wamekamatwa na hati mkato.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. JANEJELLY J. NTALE: Mheshimiwa Spika, naona muda umeniiishia lakini nitalileta kama swali naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ataniwezesha kuchangia ninayoenda kuchangia.

Kwanza nimshukuru Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na niwapongeze kwa kazi wanayofanya, wanafanya kazi kwenye mazingira magumu sana. Lakini pia naungana na Taarifa ya Kamati ya Kilimo, Maji na Mifugo asilimia 100 kwa yale yote ambayo wameshauri.

Mheshimiwa Spika, lakini mimi nijikite kwenye bajeti inayotolewa kwenye Wizara husika. Ukingalia bajeti iliyoletwa mbele yako kuombwa hapo bajeti ya Wizara yote ni shilingi 199,194,996,810; lakini uvuvi peke yake imepewa shilingi 122,350,470,000; mifugo imepewa shilingi 47,844,949,810.

Mheshimiwa Spika, ukitafuta percentage uvuvi wamepata asilimia 71.7; mifugo wamepata asilimia 28.3; ukiliangalia kwa macho ya kawaida uvuvi inaimeza mifugo, lakini hapa tunasema asilimia 60 ya Watanzania wako kwenye kilimo, uvuvi na mifugo.

Mheshimiwa Spika, lakini Idara moja ya Mifugo imemezwa na uvuvi, hapa watatokaje? Hatuwezi tukaona utendaji ulio bora kwenye mifugo lakini pamoja na bajeti hiyo kuwa ndogo, inachelewa kupelekwa kwenye Wizara na inapelekwa kwa asilimia ndogo sana, lakini tunataka mifugo na uvuvi viendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wewe ni Mbunge wa muda mrefu ndani ya Bunge hili, unakumbuka historia nyuma Wizara ya Maji, Nishati na Madini zilivyokuwa pamoja, Idara ya Madini ilikuwa inazimeza Wizara zingine idara zingine hazikuonekana kabisa zilichokuwa zinafanya. Lakini kwa makusudi ya ushauri wenu kama Bunge mkashauri Wizara zikatoka tatu mle; ikatoka Wizara ya Maji, Nishati na Madini na mafanikio tumeyaona. Mimi niombe tu kwa kiti chako Mheshimiwa Balozi juzi alichangia akasema Bunge la Kumi na Mbili nasi tutoke na alama kwenye kilimo, uvuvi na mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuishauri Serikali isiangalie gharama ichukue maamuzi magumu ya kuzitenga hizi idara mbili; uvuvi iwe na Wizara yake na mifugo iwe na Wizara yake. Baada ya kulifanya hilo utendaji unaweza ukaonekana. Kwa kweli Waziri akiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi mtu mmoja ni pasua kichwa, kwa sababu anagusa maisha ya wananchi chini kabisa kila Mtanzania anamgusa, lakini anamgusa kwa mazingira magumu sana ya bajeti kutotosha na ya kwamba kila mwananchi anatakwa aguswe. Lakini hapo hapo idara moja inapewa hela kidogo, idara nyingine inapewa hela kubwa, ni ngumu sana kufanya kazi kwenye mazingira hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili nishauri kwenye uvuvi; niliwahi kusema kwenye Mpango wa Maendeleo kwamba Tanzania tumebalikiwa kuwa na maji ya kutosha, maziwa, bahari na mito lakini bado hatujawekeza kwenye uvuvi bado hatujajikita kwenye uvuvi. Leo hii kama Serikali ikichukuwa makusudi mazima kujenga vizimba kila maziwa yetu, wakawapa wananchi hata kwa kukodisha, tukawekeza mapato yatapatikana, ajira zitapatikana na uvuvi utaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga hoja mkono ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, tumekuwa tunajenga nyumba za askari lakini kwa uchache na kasi ndogo sana. Askari kuishi na raia inapunguza heshima yao na kuleta wakati mwingine mazoea na wahalifu. Tuongeze kasi ya ujenzi wa nyumba za watumishi, lakini hata.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uweza wa kusimama hapa. Nitakuwa mwizi wa fadhila kama sikumshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alivyojipambanua kwamba yeye maendeleo kwake hayana itikadi za kivyama. Kama angefuata itikadi za vyama maendeleo tunayoyasema Dar es Salaam yasingekuwepo. Dar es Salaam tunajua fika ilikuwa ni ngome ya wapinzani lakini amefanya maendeleo ya barabara, maji, elimu iliyopelekea wananchi wa Dar es Salaam sasa nao kumlipa fadhila ya kuifanya Dar es Saalaam ya kijani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mpango, amekuja na Mpango kwelikweli kama jina lake. Hata hivyo, Mpango huu wanaohusika ni wataalam wake ambao ni rasilimali watu. Mimi nijikite kwenye rasilimali watu. Haya yote tunayoongea humu, yote tunayojadili humu, wanaoenda kuyatekeleza ni rasilimali watu, ni watumishi wetu, lakini kuna sehemu hawa watumishi hawatoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Waheshimiwa Wabunge wamesema kuhusu kilimo, lakini ukiangalia nchi ina shortage ya Maafisa Ugani 6,000 badala ya 12,000. Sasa hawa 6,000 hawawezi kutumika kwa nchi kumfikia kila mkulima, suala hili tuliangalie kwa makini. Hata hao waliopo vitendea kazi walivyonavyo ni vichache sana. Tumesikia kuna Kata zina vijiji 15, lakini Afisa Ugani huyu hata baiskeli hana, atamfikiaje huyu mkulima? Kama kweli tunataka kilimo kiwe ni uti wa mgongo, tuwaangalie hawa Maafisa Wagani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajivunia GePG ambapo mtandao uliotengenezwa na watumishi wetu wa Serikali. Hii ni software tungekuwa tunainunua kwa wataalam wengine ingetumia bilioni za fedha. Kwa hiyo, tuwaendeleze hawa watumishi wetu kielimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi imefikia wakati watumishi wanaogopa kwenda kusoma kwa sababu ya nyaraka zinazotoka utumishi. Mtumishi sasa hivi akienda kusoma, anaambiwa muda wake alioenda shule hautahesabiwa kwenye promotion yake. Sasa tunaenda kuzalisha wale walioenda kusoma na aliyebaki akaendelea na ule muundo anakuwa mwandamizi, yule aliyetoka na elimu yake anakuwa junior kwake. Sasa hii inapunguza utendaji kazi ndani ya Serikali. Huyu mwenye elimu kubwa angemshauri huyu lakini sasa huyu ni mwandamizi kwake, atamshaurije na huyu ni senior wake? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Utumishi niwaombe, tuangalie hizi nyaraka. Kuna sheria za kiutumishi, lakini nyaraka ndani ya sheria za kiutumishi zimekuwa nyingi mno, zinaleta mkanganyiko. Sasa hivi mtumishi ukimwambia nenda kasome ataleta sababu zisizo na msingi, lakini ukimfikia kwa karibu anakwambia ngoja kwanza nipande kwenye huu muundo nifikie daraja la uandamizi ndiyo nitaenda kusoma lakini sasa wanadumaa na utaalam unabadilika kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuiangalia hii miundo, tutabaki tunawalaumu wataalam hawafanyi kazi lakini kumbe kuna kitu kimewakwamisha. Naomba tuliangalie hili kwa umakini. Tuna vijana ambao ni wazalendo wa kweli. Mfano ni hii Wizara ya Fedha ambayo imekuja na huu Mpango, wanakesha, wanaumiza vichwa kuja na Mpango kama huu, lakini sasa miundo inawakamata. Tuliangalie suala hili na kama tunataka nchi hii iendelee, tuwekeze kwenye rasilimali watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ana utashi kabisa wa kuwekeza kwenye rasilimali watu. Ukiangalia Ilani ya Uchaguzi imesema hivyo; ukiangalia hotuba yake hapa imesema hivyo; Mpango umekuja unasema hivyo, lakini je, tunatekeleza sisi tunaomsaidia? Nizidi kuiomba Menejimenti ya Utumishi wa Umma, hebu angalieni nyaraka zenu za kiutumishi, zimekwamisha kabisa haya maendeleo na huu Mpango wanaoenda kuutekeleza ni rasilimali watu hii hii. Tukiyafanya hayo, Tanzania inaenda kubadilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia siku ya leo.

Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai na afya, nitakuwa mwizi wa fadhila nisipomshukuru Mheshimiwa Rais, kwa niaba ya Vyama vya Wafanyakazi kwa jambo alilolifanya la wenzetu waliyopata ajali ya kughushi vyeti kuruhusu walipwe akiba yao waliyokuwa wakichangia wao wenyewe ni jambo la kiungwana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile najikita kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kuhusu Mpango na Maendeleo aya ya 33 kipengele cha Nne, wanasema watachochea maendeleo ya watu hasa kwenye elimu, afya, maji na ardhi. Leo naenda na elimu na afya. Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ameonyesha nia thabiti ya kupigana na umaskini, ujinga na maradhi na ndiyo maana sasa hivi nchi nzima tuna zahanati 5,123, vituo vya afya 650, shule za msingi 17,181 na sekondari 4,211, hizo zinamilikiwa na Serikali tu. Hata hivyo hivi vyote havitakuwa na maana kama hatuna rasilimali watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahitaji ya wataamu wa afya ni 126,294 waliopo ni 61,304 pungufu ni 64,960, sawasawa na asilimia 52. Lakini upande wa walimu shule za msingi mahitaji ni 299,210, waliopo ni 167,245 pungufu ni 131,965 sawa na asilimia 44 hizo ni shule za msingi. Vilevile walimu wa sekondari wanahitajika 174,632, waliopo ni 84,700 pungufu ni 89,332 sawasawa na asilimia 51.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bila kuwa na rasilimali watu hii hakuna tutakachofanya na ninaona huruma kwa hela tulizoweka kwenye zahanati na shule hasa tulizojenga na COVID. Kama hakuna walimu shule zile zitageuka magofu, zile zahanati zitakuwa magofu. Haiwezi kuwa zahanati kama haina wataalamu na wale wanaoenda kutibiwa pale na bila kukazania hivi vitu adui umasikini hatutomtoa Tanzania. Naomba na nimeangalia mpango mnasema mtawaboresha watumishi lakini hamjasema mkakati thabiti wa kuajiri walimu na watalaam wa afya na hawa ndiyo wakuhudumia hivi vitu nilivyovitaja. Ninaomba huu mpango uoneshe mwaka huu kuna mkakati gani wa kuongeza kada hizi za watalaamu wa afya na walimu wetu ili hayo majengo yasije yakageuka magofu na hela tuliyoweka huko ikapotea kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe bajeti hii ituonyeshe ajira, itoke tu tutoe bajeti ya mwaka mmoja tuseme mkakati ni kuajiri walimu na watalaamu wa afya tu ili tuweze kupunguza hii asilimia hamsini na mbili na asilimia arobaini na moja. Nilikuwa na ushauri tu, ushauri wa kwanza ni hiyo Serikali kuweka mkakati wa namna ya kuajiri hizi kada mbili ili tuweze kufikia malengo tuliyoyaweka, pendekezo la pili Halmashauri zinazo vyanzo vya ndani vya mapato waruhusiwe watalaam wako wengi mtaani, waajiri kwa mkataba ili kuziba pengo hili ili tuweze kumsaidia Mama Samia Suluhu Hassani kufikia nia yake yakufuta masikini, ujinga na maradhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ni huo leo, ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami kama wenzangu wote nianze kwa kutoa pole kwa Watanzania wote na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuondokewa na Rais wetu kipenzi, Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue fursa hii nimpongeze Mheshimiwa Mama Samia Suluhu kuwa mwanamke wa kwanza kuvunja na kuweka historia ya kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Rais wa Nchi kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki na Tanzania yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza Mheshimiwa Mwigulu kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais kupewa Wizara nyeti; Wizara ya Fedha na Mipango. Hongera sana. Vile vile nampongeza kwa Mpango ambao ameuwasilisha leo yeye na timu yake yote ya waatalam pamoja na Mwenyekiti wake wa Bajeti. Kwa kweli inatoa matumaini ya Taifa letu, tunaenda wapi kiuchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita katika sehemu ya uvuvi na kilimo. Nikianza na uvuvi, Tanzania ni nchi iliyobahatika sana. Tuna maziwa ya kutosha, mito na bahari, lakini bahati hii bado hatujaitumia. Tumeenda na kudra ya Mwenyezi Mungu tu kuvua samaki walio ziwani na baharini; lakini kama tukijikita kwenye vizimba kufuga kitaalam Mheshimiwa Waziri atapata mapato ya kutosha na ugomvi kati ya Serikali na wananchi kwa uvuvi haramu utakuwa umekoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye sehemu hii Serikali ijikite kutoa hela za kutosha, Wizara husika ndiyo itafute maeneo na kujenga vizimba. Vizimba hivyo wananchi wakodishwe kufuga. Nilikuwa napiga mahesabu, lakini mimi sio mtaalamu wa hesabu; ila tukiweka vizimba hivyo kila baada ya miezi sita tunavua Samaki, tena ambao siyo wa kupima na rula, kwa sababu amefikia kiwango kinachotakiwa. Vile vile hapa tutapata kodi, hapa tunawainua akina mama na vijana, watapata ajira kutokea pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi Jirani, Uganda nimetembelea mwenyewe vizimba vya akina mama. Mwanamama anakwambia kwa mwaka ana uwezo wa kutengeneza shilingi milioni 200 au shilingi milioni 15, lakini sisi Tanzania tumekaa tu. Naiomba Serikali, nakuamini Mheshimiwa Mwigulu na Waziri wa Uvuvi, tuchukue hatua, wakati ni sasa. Mwalimu Nyerere aliwahi kusema kwamba tunaukalia uchumi, nasi tumeukalia uchumi kwenye hili la uvuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wenyewe, ukiamua wewe mwenyewe kutafuta vizimba, kuna idara inaitwa ya Idara ya Mazingira; unaambiwa hapa mazingira hayafai, hapa hayafai, lakini kwa Waganda inafaa vipi? Tunakosea wapi hapa? Sasa sisi tunaiomba Wizara husika, yenyewe ndiyo ishirikiane na Idara ya Mazingira, wote ni Serikali moja, watuambie kwamba maeneo kama haya hamtaharibu mazingira, weka vizimba, fuga Samaki. Mheshimiwa Waziri utapata mapato ya kutosha pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri, kwenye bajeti ijayo Mheshimiwa Waziri tenga ruzuku, tupe akina mama na vijana tukaweke vizimba kule tukutengenezee mapato na tuinue uchumi wa Tanzania. Huo ndiyo ulikuwa ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo, toka uhuru mpaka leo bado tuko kwenye kilimo cha jembe, hatujawahi kutoka hapo, lakini tunasema kilimo ndiyo uti wa mgongo, kilimo ndiyo asilimia 70 ya Watanzania tuko pale, kilimo ndiyo kinagusa kila Mtanzania, ndiyo tumekiweka mbali na Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri niko kwenye Kamati ya Kilimo. Tumetembelea miradi kama Kilosa, lakini ukiangalia kidogo kwenye sehemu ya umwagiliaji waliyoijenga pale na mazao yanayotoka pale na tumebahatika maziwa na mito ya kutosha, lakini bado hatujaingia kwenye kilimo cha umwangiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kilimo hicho tukiingia, mbegu hakuna. Kilio cha mbegu kimekuwa kikubwa sana. Hakuna mbegu za kutosha, hakuna wataalam wa kutosha, kwa hiyo, kwenye kilimo tunakwama hapo. Ushauri wangu tu, niishauri Serikali sasa ijikite kwenye kilimo cha umwangiliaji, lakini ijikite kabisa kwenye uzalishaji wa mbegu, tena ambazo ni za kiwango kwa kutumia utafiti, tutenge bajeti ya kutosha ya utafiti wa mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuhakikishe tunaajiri Wagani wa kutosha, hawapo. Leo hii kuna Kata nyingine zina vijiji 15 na mgani ni mmoja; lakini kwa sababu yuko TAMISEMI, wanamwambia utakaimu Utendaji wa Kata. Tumeyaona haya. Sasa Ugani anaufanya saa ngapi? Akishaenda kwenye Utendaji wa Kata, kule kuna kusimamia kuuza mashamba na kadhalika, Ugani anaacha, anaomba recategorization akawe Mtendaji wa Kata, tunawakosa Wagani namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado hata yule ambaye amejitahidi kulima yeye mwenyewe, masoko hakuna. Kuna kipindi ilitangazwa hapa zikalimwa mbaazi Tanzania kwamba zitaenda India, lakini matokeo zilipelekwa mpaka kwenye vituo vya shule kuwapikia wanafunzi, India hazikuwahi kwenda. Sasa tunakwama wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo na uvuvi, vitu hivi tukivishika, tukaviwekea mkakati kama tulivyoweka kwenye miundombinu ya barabara, Tanzania tutafika mbali. Huo ndiyo ulikuwa ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa wasaa huu wa kuchangia. Kwanza, nianze kwa kusmhukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya njema na uhai. Pia, nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi alivyoboresha hizi Wizara hasa upande wa Menejimenti ya Utumishi wa Umma, upande wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja taarifa za Kamati hizi mbili. Zote zimejishibisha na zote zimekuja na taarifa iliyokamili. Nianze na Menejimenti ya Utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza sana kwa marekebisho mnayofanya kwenye utumishi wa umma. Hata hivyo, nina machache ya kuwashauri. Leo asubuhi mmeulizwa swali kuhusu safari ya watumishi wanawake wanaonyonyesha, ule mwongozo uko vizuri kabisa lakini Maafisa Utumishi wanachokwenda nacho wanaenda pale mwisho kwenye mwongozo kwa sababu inasemwa; “Endapo hakuna mtu wa kufanya kazi hiyo.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo “endapo” imewatesa watumishi wanawake wenye watoto wanaonyonyesha kwa kiasi kikubwa sana. Nishauri, kama “endapo” inaweza ikatoka kwenye huo mwongozo basi itoke, kwa sababu si kwamba inawatesa hawa watumishi wanawake tu inatesa na wale watoto, sasa ili mtu aweze kuendelea na hizo kazi, mwisho anamwachisha mtoto kunyonya kabla hajafika miaka miwili ili aendelee na hizo kazi. Niwaombe mkaliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, limeletwa suala la njiti, ninawaomba ni wakati sasa wa kuleta sheria humu kwenye Bunge hili Tukufu ya kuwalinda wanawake hawa watumishi wanaojifungua njiti. Sheria hiyo basi iseme kwamba siku ambayo yule mtoto njiti anapokuwa amefikisha umri wa kuzaliwa, sasa ndiyo aanze kuhesabiwa likizo yake ya uzazi, lakini watumishi hawa wanahesabiwa likizo ya uzazi pale anapojifungua kumbe amejifungua mtoto njiti, mtoto yule huwezi kumwachia msaidizi nyumbani, niwaombe sasa ni wakati wa kuleta hiyo sheria ili kuwalinda hawa watumishi wenzetu wanaojifungua watoto njiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee madeni ya mishahra ya watumishi. Mheshimiwa Rais alifanya maksudi mazima, akatoa bajeti ya kulipa madeni ya watumishi, hata hivyo, leo hii bado kuna baadhi ya watumishi wanadai madeni ya mishahara tangu mwaka 2017. Sasa, sielewi utumishi mnatumia kigezo gani, madeni ya 2020, 2019 analipwa, unakuta mwingine wa 2017 hajalipwa. Yawezekana ni mitandao yenu kati ya Wizara ya Utumishi na Idara zinazojitegemea haisomani. Niwaombe mitandao yenu isomane ili watumishi hawa wapate haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende upande wa TAMISEMI. TAMISEMI mmesema ukweli kwamba utendaji kule chini umekuwa hauridhishi. Hata hivyo, nini kinafanya utendaji usiridhishe? Ni upunguaji wa watumishi walioko chini hasa upande wa Watendaji wetu wa Kata, Vijiji na Vitongoji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii baadhi ya Walimu, baadhi ya Maafisa Ugani ndiyo wamekuwa Watendaji wa Kata, Watendaji wa Vitongoji na Serikali za Mitaa. Sasa, huyu hawezi akatoa huduma kama inavyotakiwa kwa sababu yeye hiyo siyo kazi yake. Niiombe Serikali sasa, ni wakati wa kuboresha watumishi wa Serikali za Mitaa hasa kwenye Utendaji wa Kata, Vitongoji na Vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachosikitisha hata maelekezo yanayotolewa na Bunge lako, bajeti inayopitishwa na Bunge lako, haitekelezwi ipasavyo kwenye Serikali za Mitaa. Bajeti ya Serikali ilipitishwa hapa kwamba, Watendaji wa Kata walipwe posho ya 100,000. Posho hiyo imekuwa kitendawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninao mtandao na Watendaji wa Kata, kuna wengine toka posho hiyo ipitishwe hawajawahi kulipwa. Wengine wanadai miezi 11, wengine wanadai miezi 12. Si vizuri kutaja hizo Halmashauri. Nimeshakaa na Waziri wa TAMISEMI, nimemueleza suala hilo, nimekaa na Naibu Waziri wa TAMISEMI, nimemueleza suala hilo, niiombe leo Serikali kupitia Wizara ya TAMISEMI, itoe tamko kwa hizi posho za Watendaji wa Kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imefikia sehemu nyingine wanaambiwa mkakusanye ushuru wa matrekta msipofikia malengo hatuwalipi hiyo posho. Sisi hatukupitisha hiyo posho kwamba wanakwenda kufikia malengo, ni haki yao. Wengine wameambiwa hizo hela zitapitia kwenye akaunti za WDC! Hili ni jambo la kushangaza, haki ya Mtumishi anayo akaunti ya mshahara unamwambia hela yake ipitie WDC, ikishapitia WDC ataipata kwa uhakika? hawezi kuipata kwa uhakika.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watumishi wanaolipwa na own sources za Halmashauri, badala kuwa mishahara yamekuwa mateso. Kuna watumishi wengine wanakaa miezi mitatu mpaka minne hajalipwa ule mshahara. Hivi kweli tunategemea huyu atafanya kazi ipasavyo! Maana haki na wajibu vinaendana. Naiomba Serikali iangalie hawa watumishi wanaolipwa mishahara kupitia kwenye Halmashauri, wanateseka. Sasa mtoe azimio, mtoe maelekezo, kama Halmashauri haziwezi kulipa, basi ndio hawa wapate ajira za kudumu, walipwe na Serikali Kuu kama walivyo watumishi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niongelee TARURA. TARURA tumewapa kazi kubwa sana, kwa hiyo, tuwaongezee bajeti, tuwaongezee rasilimali watu, tuwape mamlaka yaliyo makuu ya kuweza kufanya hizi kazi. Utashi wa kisiasa umeingia sana kwenye TARURA. TARURA wanaweza wakasema barabara hii ndiyo ingestahili kujengwa, lakini utashi wa kisiasa ukasema ijengwe barabara sehemu nyingine. Kwa hiyo, nao wanakuwa kwenye mchanganyiko wa kushindwa kuamua ni kipi wafanye na kipi waache. Naomba kama tumeamua TARURA ndiyo ihusike na barabara za Serikali za Mitaa, basi tuamue kuongeza bajeti ya kutosha ili barabara hizi ziweze kutengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mzuri, Dar es Salaam siasa zake ni Barabara na miundombinu, lakini ukiangalia barabara zilizoko Dar es Salaam ni za kitaifa. Kwenye mitaa kule ni hatari, na tunategemea hizo barabara ndiyo zitusaidie kupata kura za wananchi. Kama tukichukua uthubutu wa kutengeneza barabara za Dar es Salaam tunaweza tukaongea mengine kwenye uchaguzi. Barabara zinatisha, hazipitiki. Nawaomba... (Makofi)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Janejelly kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mabula.

TAARIFA

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa mchango mzuri wa Mheshimiwa Mbunge. Nataka tu nimpe taarifa kwamba umuhimu wa barabara zinazojengwa na TARURA siyo kwa Dar es Salaam peke yake, ni nchi nzima, kwa sababu ushindi wa CCM utatokana na kura zitakazopigwa nchi hii na barabara zina hali mbaya. TATURA inahitaji fedha nyingi zaidi kuliko sasa. Ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Janejelly, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea, lakini nawaomba Wabunge, tunapoongelea suala la Dar es Salaam kila Mbunge atuunge mkono, kwa sababu hakuna Mbunge ambaye hana makazi Dar es Salaam ndani ya Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kabisa!

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunapoongelea suala la Dar es Salaam mtuunge mkono, mkubali barabara za Dar es Salaam zitengenezwe. Mwache kutujia inbox. Inbox wanakuja na kusema ongeleeni barabara ile, ongeleeni barabara ile, hata kwa message, lakini sasa hapa tukiongea, wanaona kama tunajipendelea Dar es Salaam. Hatujipendelei, Dar es Salaam ndiyo kioo cha Taifa, Dar es Salaam ndiyo Mji Mkuu wa kibiashara, lazima barabara za Dar es Salaam zitengenezwe. (Makofi)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Janejelly kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Lazaro Nyamoga.

TAARIFA

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tu kuweka kumbukumbu sawa, tupo Wabunge wengi ambao hatuna makazi Dar es Salaam, tunaishi majimboni, mmojawapo ni mimi. Naomba kutoa taarifa hiyo ili wananchi wasije wakaelewa tofauti na hilo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Janejelly taarifa hiyo unaipokea?

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimu sana mdogo wangu huyu, lakini hiyo taarifa siwezi kuipokea, sijasema hawakai kwenye majimbo yao, lakini nimesema wana makazi Dar es Salaam. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee na mchango wangu. Naomba Barabara za Dar es Salaam ziangaliwe kwa umuhimu wa kipekee.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naongea haya, mnafanya utani, mnanipiga taarifa, lakini Dar es Salaam tuelewe ndiyo ina asilimia 15 ya kura za nchi hii, tunazozitegemea. (Makofi)

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa, alishapewa taarifa mbili zinatosha.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachoongea ninamaanisha. Ni lazima Dar es Salaam iangaliwe kwa jicho lingine, ni lazima Dar es Salaam barabara zitengenezwe. (Makofi

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kuhusu Utaratibu.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kunipa Afya na leo na mimi nichangie kwenye bajeti ya TAMISEMI. Lakini nikupongeze Mheshimiwa Ummy kwa kuteuliwa na kuendelea kuaminika kuisaidia Serikali pamoja na wasaidizi wako. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze pia walioandaa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, hawa kweli kweli walikuwa na fikra zilizo sahihi, kwa mara ya kwanza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ukurasa 180 -181 inaongelea maslahi ya watumishi wazi kabisa, na niwashukuru waliochangia kwa kusema maslahi ya watumishi wa Tanzania. Hasa wengi mlijikita kwa walimu lakini niipongeze pia Serikali imefikia uchumi wa kati kabla ya mwaka 2025, lakini waliofanya hii kazi ni watu gani, ni watumishi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na nilipokuwa naangalia makundi yangu ya watumishi hata Wabunge mpo ni watumishi wangu wa miaka mitano mitano, lakini kuna wale watumishi wanaotoka baada ya miaka 60 kustaafu. Lakini watumishi hawa walikuwa wanafanya hivi vyote kwasababu gani, walikuwa na maagano na Serikali, Serikali kupitia vyama vya wafanyakazi iliwaomba watumishi, kwamba tuvumilie kwa miaka mitano tujenge Uchumi, baada ya kumaliza kujenga uchumi tutakuja na maslahi yenu na ndio maana Ilani ya Uchaguzi imeyasema tumezungusha hapa tunaongea matatizo ya watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa unjuka wangu mheshimiwa Jenista ulipokuwa unawasilisha bajeti yenu ya Waziri Mkuu niliangalia angalia sikuona suala la nyongeza ya mshahara lakini nikasema ngoja ninyamaze labda ndio style, TAMISEMI mmekuja na bajeti bado haioneshi ukiangalia vifungu vya mishahara kama kutakuwa na nyongeza, na jambo hili tusipoliangalia na kulisemea tunasema mtatizo matatizo lakini hatuangalii chanzo cha tatizo. Yawezekana hata kushuka kwa utendaji ni watumishi wamefika mahali wamekufa ganzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ebu tujiulize kwenye miaka mitano ni watumishi wangapi wamestaafu kwa mshahara wa zamani ambapo tunajua sheria kikokotoo hufanyika kwenye mshahara, waheshimiwa Wabunge niwaombe kwenye hili wote mni-support tuongelee suala la nyongeza ya mshahara, nyongeza ya mshahara kwa mtumishi inaongeza hata mafao yake, lakini miaka mitano watumishi hawa walivumilia ili tujenge uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumeshajenga uchumi umefika uchumi wa kati tena kabla ya muda wake, na ukiangalia mambo ya kufanyia watumishi kwenye Ilani yapo 16 sasa kama tukipita bajeti hii bila kulisema hili, ambalo limeandikwa pale naomba kunukuu; “kwamba Serikali itaboresha mishahara ya watumishi wa umma kwa kuzingatia ukuaji wa uchumi wa Taifa na tija ya wafanyakazi,” tija wameifanya watumishi wamefikisha uchumi wa kati kabla ya muda wake na uchumi umefika uchumi wa kati. Sasa tunasubiri nini kuongeza mishahara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuongeze mishahara watumishi, Waheshimiwa Wabunge na nyie linawahusu, watumishi wakiongezewa na nyie mtaongezewa kwasababu na nyie ni watumishi wa miaka mitano lakini naona tunalifumbia fumbia macho. Sasa kwa sababu nimetumwa kuwakilisha watumishi leo ngoja nilisemee hilo la mishahara ya watumishi na nimeona Waziri wa Fedha anaondoka na begi lake lakini nadhani atanisikia alipo kama bajeti yake itakuja haina nyongeza ya mshahara… (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ngoja ngoja Mheshimiwa Janejelly, waheshimiwa wabunge huwa narudia mara kadhaa, Mbunge unapochangia zungumza na kiti na sio Mawaziri.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

NAIBU SPIKA: Kwasababu ukizungumza na Waziri asipofanya usije ukalidai Bunge, ongea na kiti ndicho kinachotunza kumbukumbu ni nani ambaye ameomba kitu gani. Hata Mheshimiwa Ummy hapa akinyanyuka akaenda usiseme Waziri ametoka namsubiri atayapata tu, kwa hiyo, wewe zungumza na mimi usimwangalie Waziri yupo katoka taarifa zake atazipata.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niongee na kiti chako, niseme hivi kama Wizara ya Fedha ikija haina nyongeza ya Mishahara ya watumishi kwa kweli kwa bajeti hiyo wabunge mni-support tukamate shilingi watumishi wanaumia kwa nyongeza ya mishahara na yawezekana haya yote tunaona utendaji unashuka, Wakurugenzi wanafanya vibaya, unajua msongo wa akili unaweza ukafanya, ukafanya mengi, yawezekana wengine wanakaa kimya, wengine wanakuwa na hasira lakini wengine wamedumaa utendaji umedumaa. Hapa nina meseji nilikuwa ninazisoma watumishi wanasema miaka mitano tuliyoahidiana imekwisha kuja jambo letu ebu liongee jambo letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na jambo la watumishi ni nyongeza ya mshahara, jambo la watumishi ni kupandishwa vyeo, jambo la watumishi ni kuangalia hayo maslahi yao, nguzo yao kubwa ni mshahara maisha yanapanda, kodi za nyumba zinapanda ada za shule zinapanda lakini mshahara upo vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee na suala la walimu hakuna mtumishi anayeumia kama mwalimu na hii haina mwalimu yupo Dar es Salaam haina mwalimu yupo Tabora. Walimu sasa hivi nauli ya likizo imekuwa ni kitendawili, ni neno gumu kwenye kamusi mtu anakwenda likizo tatu nne hajawahi kulipwa nauli ya kwanza ya likizo. Wakistaafu nimeshuhudia Mkurugenzi mmoja anawaambia nitawatafutia roli sasa, na hakunijua kama ni Mbunge wa Wafanyakazi lakini nilimwambia hakuna mwalimu atakayekwenda na roli, alisema nitawapakia kwenye roli sina fedha TAMISEMI hawajaleta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwalimu aliyefanya kazi akafikisha umri wa miaka 60 leo unamwambia utampeleka na roli, utampeleka na roli wapi lakini wanawapiga dana dana akienda Manispaa wanamwambia TAMISEMI ndio wana fedha zako, akienda TAMISEMI wanamrudisha. Jana nilikuwa na walimu ambao ni tatizo wanaongezwa vyeo lakini mishahara haibadilishwi, mpaka amefikia kustaafu wapo watano na ni Manispaa ya Ilala inabidi niseme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wamenifuata Bungeni hapa wamelipwa pensheni lakini wa mishahara ya zamani lakini Manispaa inawaambia mfuko ndio una tatizo, namshukuru sana Mkurugenzi wa Mifuko, tumeenda pale ametupokea aka-print barua zote ambazo alikuwa anaandikiana na Manispaa kwamba ebu lipa mapunjo yao, lipa faini mnazotakiwa hawa wapewe tofauti zao. Lakini ebu fikiria mstaafu amepanda gari kutoka Dar es Salaam mpaka Dodoma na unamdanganya tu unamwambia mfuko ndio unashida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu walipandishwa vyeo miaka sita mtu hakubadilishiwa mshahara na amefikia kustaafu. Naomba Wabunge tuwe wakali Wabunge kazi yetu ni kuishauri Serikali tuwashauri haya wayaangalie na sio kwa walimu yanawapata watumishi wengi, watumishi wengi, wengi mno wapo kwenye tatizo hilo la kulipwa pungufu ya pensheni kwasababu wanapopandishwa madaraja mishahara yao haibadilishwi lipo kabisa hilo. (Makofi)

Mheshimia Naibu Spika, mwisho naunga mkono hoja lakini tuliangalie la nyongeza ya mshahara naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, Ahsante kwa kunipa nafasi hii kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kupata nafasi ya kusimama hapa nami kutoa mchango wangu. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri na Naibu wake na watendaji wake jinsi mnavyofanya kazi.

Mheshimiwa Spika, nilianzia kazi maji miaka ya1987 ukilinganisha na leo kweli Serikali imefanya kazi kwenye maji haikuwa hivi. Lakini kwasababu watu wengi wameshaongelea maji, matatizo ya maji na kila kitu mimi naomba nijikite kwenye miundombinu na mapato ya mamlaka zetu za maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunajua kuna nyumba za Serikali nyingi, Tanzania nzima nyumba hizi kwenye bill za maji huwa hazilipwi kule kwenye nyumba za Serikali kwenye bill zile. Sasa tuanze kuzifungia prepaid nyumba hizi kuokoa mapato ya Mamalaka za Maji yanayopotea kumekuwa na uzoefu baadhi ya watumishi wa Serikali au baadhi ya viongozi wanahama wanaacha bill kwenye nyumba zile bila bill zile kulipwa sasa hii inakuwa ni hasara kwa Mamlalaka za Maji, wakati mwingine inakuwa ni hasara kwa mtu anayeingia kwenye nyumba ile kuambiwa alipe zile bill ambazo ziliachwa kule.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapitisha bajeti ya kila taasisi hapa ikiwa na gharama za ulipaji umeme na maji, lakini nadhani kwasababu ni Serikali yenyewe kwa wenyewe Wizara ya Maji mnaona aibu kwenda kukata maji kule kwenye zile Taasisi na hawachukuli umuhimu wa kulipa bill za maji. Sasa niwashauri nishauri Wizara ya Maji anzeni kufunga prepaid mita kwenye taasisi za Serikali ili kuokoa yale mapato, tukishafunga hizo prepaid watalipa kama inavyotakiwa na ukiangalia hata kwenye ripoti ya CAG mapato mengine ya maji yanapotea pale taasisi za Serikali azilipi ipasavyo bill za maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu twende tukafunge prepaid kwenye hizo taasisi za Serikali walipe kwasababu bajeti ipo, Mheshimiwa Spika unaipitisha hapa na Wabunge tunapitisha ulipaji wa gharama zozote za uendeshaji wa Ofisi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite tena kwenye miundombinu, Wizara ya Maji au Mamlaka za Maji wanapokuwa wanafunga yale mabomba ya maji watayapitisha kwenye barabara, ujenzi wa barabara ni gharama kubwa nayo kwa Serikali. Sasa niombe tu Wizara hizi mbili wakati mnapoanza ujenzi wa miundombinu mkae pamoja mshauriane kwamba ni wapi miundombinu itapita ili tupunguze gharama za utengenezaji wa barabara zinazobomolewa wakati wa kupitisha mabomba ya maji. (Makofi)


Mheshimiwa Spika, kuna miundombinu ya haya mabomba kuchakaa na kumwaga maji hasa kwa jiji la Dar es Salaam hiyo ndiyo ilikuwa kubwa sana maji yanamwangika hovyo. Niombe tu Wizara ya Maji, tumesema chuo cha Maji sasa havi kinatowa wale vijana hawajapata kuzunguka na kuangalia yale mabomba ambapo maji yanapotea wakafanye kazi ya kuwa wanatoa taarifa mabomba yale yanafanyiwa matengenezo ili maji yasipotee na watumiaji wa maji wasipate bill kubwa.

Mheshimiwa Spika, ninachojua Wizara ya Maji Mamlaka zenu za Maji ni maji salama na safi na maji taka, sasa mnapokua kutengeneza ufungaji wa maji basi fanyeni na ufungaji wa mabomba ya maji taka viende pamoja ili kuweza kufanya hivi vyote vitu viwe pamoja kupunguza gharama na kuweka na kuweka sehemu za miji kuwa salama zaidi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo niongeze tu kama mtumishi wa wafanyakazi kuna wakurugenzi wengi sasa hivi wanakaimu, mnawatumishi wengi wanakaimu, kukaimu nafasi huwa kunapunguza ushujaa au confidence ya kufanya kazi, basi niombe wale ambao mnaona wamefanya vizuri tunajua sheria inasema akaimu miezi sita, kama unaona ajatosheleza basi mtowe weka mwingine, kama unaona amestahili na amefanya vizuri basi watumishi hawa ambao ni ma-engineers wapeni hizo confirmation ili wawe na uhakika wa kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga hoja mkono ahsanteni sana.

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, nami namshukuru Mwenyezi Mungu kupata fursa ya kuchangia kwa maandishi katika Wizara ya Afya. Nimshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi za makusudi anazofanya kwa ajili ya kuimarisha huduma ya afya hasa afya ya mama na mtoto.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Ummy Mwalimu ambaye amekuwa mwalimu kama jina lake lilivyo hasa kwa masuala ya afya, tunakuamini endelea kumsaidia Mheshimiwa Rais. Pia nimpongeze Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Mollel kwa jinsi anamsaidia pamoja na wataalam wote wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, niombe sasa nijikite kwenye mchango wangu katika Kiwanda cha Viuadudu kilichopo Kibaha, Pwani. Suala kubwa katika kiwanda hicho ni soko na mnunuzi mkuu ni Wizara ya Afya. Kwa msingi huo naomba kushauri yafuatayo; Wizara ya Afya na TAMISEMI wasukumwe kusaini mikataba wa manunuzi; ili mkataba utekelezwe Wizara ya Afya itenge bajeti kuendana na mahitaji na Wizara ya Fedha itoe fedha kwa mchanganuo utakaoianishwa kwa manunuzi ya kila mwezi; na fedha ya ithibati itolewe ili kiwanda hiki kiweze kupata soko la nje;

Mheshimiwa Spika, haya yakifanyika lengo la kiwanda hiki na nia ya kujengwa itaonekana.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JENEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu yake kwa kazi nzuri mnayoifanya kuendeleza kilimo.

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye block farm katika mazao ya kimkakati. Tunajua wana mazao ya kimkakati kila mkoa. Mathalani zao la kimkakati la Dodoma tunajua ni zabibu na alizeti, lakini kama tungetafuta block farm, tukawagawia wakulima, tukaweka miundombinu mizuri pale, itawasaidia sana hawa wakulima kuweza kuwakopesha hata mikopo ya kuendeleza kilimo na kuwapa wataalamu wa kuwasaidia katika kilimo kile. Kwa sababu watakuwa wako pamoja, wanahudumiwa kwa pamoja na wanaweza tukazalisha vya kutosha kwa kutumia block farm. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hizo block farm zitatusaidia kupata masoko kwa sababu, patakuwa panafikika kwa wale wateja wanaohitaji kununua mazao yetu. Tuna imani tutakuwa tumeweka miundombinu ya kutosha ya barabara, tutakuwa tumeweka wataalamu wa kuweza kuwasaidia watu kwenye kuuza mazao, tutakuwa tumepafanya mahali ambapo ni pa soko la kuweza kuuza mazao yetu haya. Kama hatukufanya hivyo, kwa kweli tutakaa kwenye kilimo cha ndoto ndani ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, juzi wakati unasainiwa Mkataba wa Mafuta, Kiongozi Mkuu wa Nchi ametuambia, Tanzania tukitaka kuendelee tuwekeze kwenye kilimo cha biashara, kwenye nishati na kwenye miundombinu. Sasa ifike wakati basi, tuone hizi block farms ndiyo za kututoa mahali tulipo. Hii ya kumfuata mkulima mmoja mmoja, tutachelewa kwa sababu, kwanza wataalamu wa kutosha hatuna, miundombinu kuwafuata wakulima huko waliko, ni ngumu zaidi na uwekezaji wake utakuwa mkubwa zaidi, lakini tukiwaweka pamoja, tukawahudumia kwa pamoja tunaweza tukatoka hata kwenye sakata hili la ukosefu wa mafuta, ukosefu wa masoko na wakulima wetu wakapata thamani ya kile wanachokilima.

SPIKA: Mheshimiwa Jenejelly, mnaposema block farm mnamaanisha nini?

MHE. JENEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ninaposema block farm naamisha hivi, kwa mfano Dodoma kuna ardhi ya kutosha, kwa hiyo, Serikali iende pale impimie kila mkulima. Kwa mfano, kama ilivyo Singida, katika zao la korosho wamepimiwa na kila mkulima ana sehemu yake, ana eka zake za kulima, lakini wote wako kwenye sehemu moja ambayo ni rahisi wataalamu kuifikia, ni rahisi kupata pembejeo, ni rahisi kutengeneza miundombinu ya pale na ni rahisi kutafuta soko la mahali pale kwa sababu wako sehemu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndiyo ilikuwa maana yangu. Hilo ndilo litakalotutoa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, tukienda kwenye kilimo cha umwagiliaji, nacho tuangalie ambapo tumeweka miundombinu ya umwagiliaji na hawa wakulima nao ziwe ni block farm, wawekwe kwa pamoja. Tumeona hapa Tume ya Umwagiliaji tunaambiwa imefikia wakulima 714, bado tuko mbali sana; kwa nchi nzima kufikia wakulima 714 wakati tunasema asilimia 70 ya Watanzania ni wakulima, bado tuko mbali sana. Najua Waziri na Naibu wake na timu yake mnajitahidi sana, lakini tuendelee kujitahidi.

Mheshimiwa Spika, haya yote yatafanyika wakipelekewa bajeti yao ya maendeleo kama tunavyoipitisha leo. Wanajitahidi sana, lakini wanakwama kwa rasilimali fedha, hatujawa serious kwenye kilimo kama tulivyokuwa kwenye miundombinu ya barabara. Ukiangalia bajeti ya miundombinu huwa inapelekwa asilimia 80 mpaka 70, lakini ukienda kwenye kilimo, tumeona wanapelekewa asilimia 18, 19, 20 au 26; hawawezi kufanya chochote. Kila siku tutamlaumu Waziri wa Kilimo, Naibu wake na wataalamu wake, lakini hatujawawezesha kwenye rasilimali fedha tukaweza kufanya kilimo kiweze kuwa uti wa mgongo kama kweli tunavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo ulikuwa mchango wangu. Tukijikita kwenye hilo tutakwenda vizuri sana.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya ufinyu wa muda niombe kuleta mchango wangu kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, niIpongeze Serikali kwa ajira ambazo imetoa kwa kipindi cha miaka miwili, lakini nitoe ushauri kwenye ajira kama ifuatavyo: -

Kwanza imefika wakati sasa tujikite na kwenye ajira za kada ya uchumi, maafisa mipango, na kadhalika, hawa wamesahaulika.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2020 Menejimenti ya Utumishi ya Umma walitoa kibali cha kuajiri wahandisi kuwa walimu wa shule za ufundi kama Ifunda, Moshi Technical na kadhalika. Vijana hawa 60 miundo ya ualimu hasa Tume ya Walimu haiwatambui hivyo hawana barua za ajira, hawawezi kuthibitishwa kazini. Niombe suala hili litafutiwe ufumbuzi.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye kitu muhimu ambayo ni Bajeti ya Serikali. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwigulu, mzee wa Yanga na Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Masauni, mzee wa kimyakimya na timu ya wataalam wote wa Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakika bajeti hii imeonyesha Wizara ya Fedha ina wachumi waliobobea. Wamekuja na bajeti ambayo imegusa kila kundi la Mtanzania. Ukiangalia vijana wameguswa, wazee wameguswa, wafanyabiashara wameguswa na akinamama wameguswa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze pia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama Samia Suluhu. Usiposhukuru kidogo hata kikubwa huwezi kushukuru, kwa masuala ambayo amefanya kwa watumishi wa Tanzania. Mimi nijikite kwenye hotuba aya ya 44, maslahi ya watumishi. Akiwa kwenye Mei Mosi alisema, atapunguza Pay As You Earn, itabakia tarakimu moja ambayo ni nane na amefanya hivyo. Alisema atafuta tozo asilimia sita kwa mikopo ya vyuo vikuu, amefanya hivyo.

Vilevile ametoa bilioni 449, kwa ajili ya kupandisha madaraja ya watumishi, si kazi ndogo hii. Mpaka sasa ripoti za leo watumishi 78 wameshapandishwa madaraja, kati ya watumishi 92,619 ambao wanatakiwa kupandishwa. Kwenye hili ni lazima nitoe ushauri kidogo kwa Serikali, kwenye upandishaji wa vyeo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Waziri wa Utumishi watatusaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upandishwaji wa vyeo, kuna kasoro kidogo imetokea. Tunakumbuka 2016 watumishi walipandishwa madaraja, lakini muda kidogo yakafutwa, wakanyang’anywa zile barua za kupandishwa vyeo. Sasa, zoezi hili lilivyoanza, imekuwa ni adhabu kwao, wanahesabika walipandishwa 2017. Kwa hiyo, hawana sifa ya kupandishwa vyeo sasa hivi na watumishi wengine wameshakaa miaka 10, lakini barua waliyonyang’anya ilikuwa ni Serikali yetu Tukufu. Kwa hiyo, tuombe hilo wajaribu kurekebisha kidogo, hawa watumishi wafikiriwe, ambao walikuwa mwaka 2016 wako kwenye haki ya kupandishwa vyeo, lakini walipandishwa halafu wakanyang’anywa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuje kwenye michango ya Mifuko. Niishukuru sana Serikali, wamekuja na muarobaini wa kwenda kuponya wastaafu wetu. Wanapoamua kwamba makato watabaki nayo na watayapeleka kwenye Mifuko. Hata hivyo, niwaombe Serikali yangu Tukufu na Waziri wa Fedha, fedha hizi wakishabaki nazo ziende kwa wakati. Tusije tukasababisha malipo mengine ya penalty kwa kuzichelewesha na tusije tukasababisha wastaafu wetu kuchelewa kupata maslahi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna madeni ya wafanyakazi yanayosababishwa na upandishwaji wa madaraja. Kuna watumishi ambao walipandishwa mwaka na 2018 na 2016, bado hawajalipwa tofauti yao, kati ya mshahara wa zamani na mshahara mpya, yamekuwa ni madeni sugu. Tuombe hili nalo Wizara ya Fedha, maana ndio wahakiki wa madeni, basi wakawalipe watumishi hawa wafaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Mfuko unaitwa Mikopo ya Usafiri kwa Watumishi wa Serikali, mikopo ambayo haina riba. Mfuko huu uko chini ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha. Tuiombe Serikali yetu wakae watafute namna ya kuuongezea fedha huu Mfuko, ili watumishi wote sasa waweze kufaidi matunda ya Mfuko huu. Fedha imekuwa haitoshi kwa hiyo, wengine wanasikia historia tu kwamba kuna mikopo ya magari yawawezeshe kuja kazini na kurudi nyumbani, lakini hawajawahi kupata mkopo huu. Ni kwa sababu, Mfuko umepewa fedha kidogo. Kwa hiyo, tuombe hapo fedha iongezwe kwenye huo Mfuko ili watumishi waweze kufaidi matunda ambayo wamewawekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niongelee suala la Madiwani ambao watalipwa moja kwa moja kutoka Serikali kuu. Kwenye halmashauri kama tunasema hawa Madiwani watalipwa na Mfuko wa Serikali kuu, tuangalie na wale watumishi ambao walikuwa wanalipwa moja kwa moja kutoka kwenye halmashauri. Watumishi hawa wamekuwa wanakopwa sana, lakini walivyolishughulikia kama Serikali, manispaa za mjini ndio waliwahi kuhamisha watumishi wao wakalipwa na Serikali kuu, lakini wa pembezoni mpaka sasa hivi, wanalipwa kutoka kwenye vyanzo vya mapato vya halmashauri. Hasara wanayopata, hawawezi kupewa bima ya afya, hawawezi kuwa kwenye pension watumishi hawa. Sasa nao tuwasaidie waweze kufaidi matunda ya Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye malipo ya Watendaji wa Serikali za Mitaa. Tumeamua kuwalipa Madiwani, Watendaji wa Serikali za Mitaa, lakini tumesahau Wenyeviti wetu wa Vijiji na Serikali za Mitaa. Hawa ndio huanza na wananchi wetu from zero, lakini Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa au Mwenyekiti analipwa shilingi 30,000 kwenye Manispaa zingine, pengine shilingi10,000 yaani haina standard. Hata hiyo yenyewe kulipwa inaweza ikapita miezi sita, hajawahi kulipwa. Suala hili linawaondolea heshima na uimara wa kufanya kazi na wanakuwa wana wasiwasi wa kufanya kazi. Kwa hiyo tuombe Serikali hawa watu nao iwaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nimshukuru sana Mheshimiwa Mwigulu, Tunamwamini, kwamba bajeti hii tukiipitisha, itaenda kwa wakati kwenye manispaa, kwenye mikoa yetu na kwenye majimbo yetu ili ikafanye kazi kama ilivyopitishwa. Tuna uhakika huu upandishaji wa watumishi, fedha zitabaki watapandishwa wenye haki za kupandishwa, lakini wakiangalia ile kasoro ambayo tumeisema ya 2016. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga hoja mkono mia kwa mia. Ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza, nimshukuru Mwenyezi Mungu anisaidie kwa haya nitakayochangia kwa manufaa ya Taifa la Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kumpongeza Waziri wa Kilimo, Prof. Mkenda, Naibu wake Mheshimiwa Bashe, Katibu Mkuu na wataalamu wote wa Wizara ya Kilimo kwa jinsi mlivyotupitisha kwenye Itifaki hii na tukaweza kuelewa. Hata ambao hatukuwa wanasheria mliweza kutubeba vizuri sana na tukaelewa. Nimpongeze pia Mwenyekiti wangu wa Kamati na niungane naye moja kwa moja kuunga mkono maoni yote ya Kamati yaliyowasilishwa mezani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie kiti chako kuwaomba Wabunge Wabunge lako Tukufu tukubali kuingia kwenye Itifaki hii ya Afya ya Mimea, Wanyama na Mifugo kwa usalama wake. Sababu zinazonifanya niwaombe tukubali ni kwa mustakabali wa Taifa kwa mazao yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia jiografia ya Tanzania tuko katikati ya nchi zote kimpaka lakini Mungu katubariki kwa ardhi yetu yenye rutuba, ardhi ambayo inaweza ikaotesha kila zao. Ukiangalia kwa Afrika Mashariki sisi ni wakulima wakubwa wa mahindi, mpunga na hili zao la parachichi ambalo limeongezeka ambalo ni dhahabu ya kijani. Sasa bila kuwa na Itifaki ya kulinda mazao yetu tutakuwa tunaibiwa kila wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano leo hii maparachichi yetu yananunuliwa Njombe yanapelekwa Kenya yanawekewa label yanapelekwa kama ya Wakenya, lakini kama tutakuwa tumejiunga kwenye hii Itifaki tuna uwezo wa kuwaambia na ku-harmonize nao kwamba hapana mkinunua kule lazima yaende na label ya Tanzania, kwa hiyo Itifaki itakuwa imetusaidia kwa aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuna kilimo cha mbogamboga ambapo mikoa yetu yote iliyo mipakani inaweza ikalima mazao hayo mfano, Kigoma, Kagera, Arusha na Kilimanjaro tunaweza tukaotesha mazao ya mbogamboga na kuweza kuyauza kwa nchi za Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna mazao ya maua vilevile ambayo yanaoteshwa Kilimanjaro na Arusha, ni Mikoa ambayo ipo mpakani ambayo Itifaki hii itatusaidia maua yetu yasiwe yanapelekwa nchi nyingine yanakwenda nchi za Ulaya na Asia yakionekana yametoka kwa nchi hizo kumbe yametoka Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hasara ambazo tunaweza kupata bila kuingia kwenye hii Itifaki ni kwa sababu ya kuwa sisi tutakuwa tunatembea peke yetu, lakini hata kwenye kitabu cha Mungu kwenye Amosi 3:3 imesema; watu wawili msipotembea pamoja hamuwezi kupatana. Kwa hiyo hii Itifaki itupeleke basi tukapatane na Afrika Mashariki nzima, tuweze kwenda kwa pamoja, tuweze kutetea mazao yetu, mifugo yetu na uvuvi wetu wa samaki, kwa sababu tumebarikiwa hata sisi ndio tuna Maziwa, Mito na Bahari kwa asilimia kubwa sisi ndio tuna maji mengi hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunavyokuwa hatuko kwenye Itifaki, kwa mfano ukienda Mkoa wa Kagera boti nyingi za Uganda zinakuja kuvua Kagera na kupeleka samaki wetu, lakini kama tungekuwa tumeshajiunga na tuna Itifaki hii tuna uwezo wa kukaa nao mezani na kuongea nao kwamba wasifanye hicho wanachokifanya basi, wavuvi wa kwetu ndio wavue tuuze ndani ya Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niwaombe Wabunge wenzangu kwa hizo sababu nilizozitaja tukubaliane kwa pamoja kwenda kwenye Itifaki hii, hata sisi tulikuwa tuna wasiwasi kwa nini imechukua muda mrefu lakini tumeelezwa ni kwamba nchi ilikuwa kwenye kujiridhisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa majira na wakati huwa yana wakati wake, umefika wakati ambapo Taifa limejiridhisha sasa kwamba tunaweza tukaenda kwenye Itifaki tukiwa tumejiandaa kwa mfano kwenye mimea tayari wamekuja na sheria tatu zitakazotulinda kwenye Itifaki hiyo. Lakini hata kwenye mifugo na uvuvi tumeielekeza Wizara ya Uvuvi na Mifugo, nao waandae sheria sasa zitakazotulinda kwenye Itifaki hii nao wameahidi watazileta haraka sana kwako, ili Bunge lako lizipitie, basi twende kwenye Itifaki hii tukiwa salama kwa kulinda Watanzania na mali zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kupata nafasi ya kuchangia kwenye bajeti ya Waziri Mkuu. Kwanza, nampongeza Waziri Mkuu kwa uwasilishaji mzuri ambao ume- cover mambo yote ya Kitaifa. Pia nampongeza Mheshimiwa Mama Samia kwa jinsi alivyoendelea kuinua maisha ya watumishi; na aliyowaahidi yote alitekeleza. Nina imani kubwa hata lile alilowaambia la mishahara, basi mwaka huu litatekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu nitajikita ukurasa Na. 58 aya 107. Tunashukuru sana bajeti ya Waziri Mkuu imekuja na vitu vyote walivyofanya, jinsi walivyokagua mikataba ya kazi, jinsi walivyokagua Usalama, lakini kuna jambo wamelisahau ambalo ni muhimu sana kwenye ushirikishwaji wa watumishi. Hawajatuletea taarifa ya Mabaraza ya Wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mabaraza haya yako kisheria kwa Tamko la Rais Na. 1 la Mwaka 1970. Mwalimu Nyerere alishaona mbali kuhusu ushirikishwaji wa watumishi. Ofisi ya Waziri Mkuu kina kitengo ambacho kinakagua Mabaraza ya Wafanyakazi; na CAG sasa hivi anakagua ukaaji wa Mabaraza ya Wafanyakazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachofanyika kwenye baadhi ya taasisi na Wizara, Mabaraza hayafanyiki kisheria inavyotakiwa. Wanafanya Baraza moja la Kupitia Bajeti kwa sababu wanajua isipopitishwa, haitapitishwa hapa Bungeni, lakini lile Baraza la kupitia utekelezaji wa bajeti na kupanga mikakati ya taasisi au Wizara, hayafanyiki.. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaweza tukawa tunasema bajeti hazitekelezwi vizuri, watumishi hawafanyi kazi vizuri, lakini ni kwa sababu hawapati ule ushirikishwaji. Hawapangi ile mikakati ya taasisi. Baadhi ya Wizara wanachofanya, wanafanya siku hiyo hiyo mabaraza mawili. Nimekaa huko, nimeishi huko najua. Wanaanza na utekelezaji, kesho yake wanafanya upitishaji wa bajeti.

Je, sasa mikakati waliyopanga itaingia kwenye bajeti wakati bajeti imeshapitishwa? Naomba Ofisi ya Waziri, kuhusu Mkuu ukaguzi wa Mabaraza, mkayakague kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee mifuko ya jamii. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais, amepeleka fedha kweli kweli kwenye mifuko ya watumishi ili wastaafu wetu walipwe. Hata hivyo, wastaafu wamebaki na changamoto mbili, huwa zinaniumiza sana. Mtumishi kabla hajastaafu kwa hiyari, Serikali humpa barua kwamba ujiandae kustaafu kwa miezi sita; lakini inapompa barua, haijiandai kutafuta zile documents zake zinazotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mtu kaanza kazi mwaka 1970, leo akifikia kustaafu, unamwambia barua ya kuajiriwa atafute yeye, kuthibitishwa kazini atafute yeye, ya cheo cha mwisho atafute yeye. Atavipata wapi? Mtumishi huyo ameshahama zaidi ya taasisi kama kumi, anaipata wapi barua ya ajira ya kwanza? Anapata wapi barua ya kuthibitishwa kazini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwashauri tu, mnapompa barua ya miezi sita ile kwamba unaenda kustaafu, pangeni na zile documents zake peleka kwenye mfuko, tuwasaidie hawa wastaafu wetu kuumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingineni ya kutokupeleka makatako ya watumishi ipasavyo.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kumpa taarifa mwongeaji kwamba siyo tu documents zinazotafutwa kwenye maeneo mbalimbali, imefika wakati mtumishi anaacha kazi, halafu anaenda kudai pensheni yake, wanamwambia tajiri yako alikuwa hajalipa michango, kwa hiyo, hatuwezi kukupa hata pensheni. Kwa hiyo, kwa kweli ni jambo gumu sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Janejelly, taarifa hiyo.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea hiyo taarifa na ndiyo point niliyokuwa naenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Taasisi na Wizara hazipeleki makato ipasavyo; wanakaa, hawapeleki. Kwa hiyo, mtumishi anapofikia kustaafu, akienda kwenye mfuko, anaambiwa una gap la miaka miwili, una gap la miaka mitatu; shughulikia. Sasa huyu ameshatoka ofisini na nafasi yake imeshachukuliwa, anashughulikia kupitia wapi? Kwa nini kwenye hiyo miezi sita mwajiri asiangalie kama mtumishi wake anayo hayo mapengo akayaziba mapema? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba Ofisi ya Waziri Mkuu, mifuko iko chini yenu, hebu mjaribu kupeleka hata maelekezo ndani ya Wizara na Idara za Serikali wawasaidie hawa wastaafu kupanga vitu vyao kabla hawajastaafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine, anapopandishwa daraja, hawarekebishi; na hili suala liko kwa watumishi wa Halmashauri na walimu. Sasa anafanyiwa kokotozi kwa cheo kile kilichokuwa cha zamani, analipwa malipo pungufu, sasa kuja kupata hiyo tofauti itamchukuwa hata miaka minne au mitano au anafariki kabla hajalipwa. Naomba na hilo mliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye michezo. Mheshimiwa Waziri Mkuu ni mwana-sports namba moja, lakini hii michezo ya Idara ya Wizara za Serikali tumeifanyia utani. Leo hii bajeti zote zitapita hapa, lakini angalia kila Wizara imeweka bajeti kiasi gani kwenye michezo? Michezo hii ina faida kwa watumishi, huwa inatufanya tunafahamiana, tunashirikiana na tunajenga afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yalipokuja maelekezo ya Katibu Mkuu Kiongozi kwamba kila Wizara ishiriki michezo, sasa taasisi nyingine wanachofanya, wanapeleka mshindani wa baiskeli mmoja na wacheza bao wawili. Wanasema taasisi imeshiriki na Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupitia kiti chako, Ofisi ya Waziri Mkuu itilie mkazo hili la michezo ndani ya Idara za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, asubuhi hapa Menejimenti ya Utumishi wa Umma wamejibu swali kuhusu watumishi waliosimamishwa kazi na kesi zao hazijaisha. Zinachukuwa muda mrefu; miaka mitatu mtumishi yuko nyumbani anasubiri hatma ya kesi yake. Mtumishi huyu anaporudi kazini, utendaji umekwisha, muda wa kustaafu umefika; na hapa katikati mnapoteza ambapo angeweza kupata hata promotion nyingine, anastaafu kwa cheo cha chini, lakini ni kwamba eti evidence hamna. Sasa kama ushahidi huna, ulimsimamishaje huyu? Naomba tuangalie hawa watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nilikuwa Serikali Kuu, lakini kipindi ambacho nimekuwa Diwani kwenye Halmashauri, nimegundua mengi kwenye Halmashauri zetu, watumishi wananyanyaswa kiajabu. Naomba tu, ukiangalia watumishi wa Halmashauri, mwajiri ni TAMISEMI, mpandisha daraja ni TAMISEMI, lakini ikifika nidhamu, tunasema Baraza la Madiwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tuliangalie kwa makini sana hili. Hata nidhamu yao irudi kwa yule anayemwajiri. Tunawaumiza sana watumishi ambao wako Halmashauri. Naomba hili tuliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, tuangalie mahusiano ya viongozi na watumishi wao. Viongozi wengi wamekuwa ni watoa maelekezo, sio wa kushauriwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono. Ahsante.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante; na mimi nimshukuru Mwenyezi Mungu kupata nafasi ya kuchangia kwenye bajeti ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Pia nimshukuru Mwenyezi Mungu ambaye alimwongoza Mheshimiwa Rais na kutuletea Jenista Mhagama kuwa Waziri wa Utumishi. Nasema hivyo nina maana gani, Mheshimiwa Jenista tumekuwa naye kwenye vyama vya wafanyakazi, lakini masuala mengi tulikuwa tukimwambia anasema lazima nishauriane na Waziri wa Utumishi, na sasa amepewa mtoto alee mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nifikishe salamu za watumishi wa Tanzania wakimpongeza Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan. Wanampongeza kwa sababu gani; kwa mwaka mmoja ametoa Shilingi bilioni 300 ili watumishi wapandishwe madaraja, ametoa Shilingi bilioni 23 ili watumishi walipwe malimbikizo ya mishahara yao. Amepunguza kodi kutoka asilimia tisa kwenda nane. lakini kwenye mfuko wa jamii amepeleka Trilioni 2.17 ili wastaafu walipwe. Hakika amejipambanua kwamba yeye maono yake ni kuendeleza maslahi watumishi wa Tanzania, Mungu ambariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa msingi huu leo nitashauri, na ninajua Mheshimiwa Jenista haya utayachukua na utayafanyia kazi nakuamini. Ushauri wangu ni kwenye upandishwaji wa madaraja kwa watumishi. Mmesema mtaendelea na zoezi la kupandisha madaraja watumishi wa Tanzania lakini upandishwaji huu una mambo matatu yote yanaongelea kupandishwa watumishi.

Mheshimiwa Spika, kuna Public Service Act Part II 6 (a) inaongelea upandishwaji wa madaraja na ujazaji wa nafasi zilizo wazi, imetaja vigezo kabisa. Lakini mwongozo wa 2013 unaendana na Public Service Act. Sasa, kuna mwongozo wa mwaka 2019, huu ndio ulikuja na kuumiza watumishi na umeruvuga mambo fulani kwenye utumishi. Mwongozo huo unasema, mtumishi aliyeanza kazi kupanda cheo ni miaka mitano, mmoja kuthibitishwa kazini minne ya kusubiri; hii ni sawasawa na umri wa mtoto kuanza shule. Lakini aliye kazini miaka minne, aliyeenda masomoni muda wake umepotea, hata pandishwa. Sasa Mheshimiwa Jenista mnaenda kupandisha watumishi vyeo, nitaomba wakati unakuja kuhitimisha uniambie mtatumia mwongozo upi kati ya hii mitatu. (Makofi)

Niende kwa watumishi ambao wanakuwa wamepewa teuzi za mamlaka ya Mheshimiwa Rais. Teuzi hizi zinapokoma watumishi hawa wanachelewa kupangiwa kazi, na kwa sababu hiyo kunakuwa kuna hasara mbili; kwa upande wa Serikali kunakuwa na hasara ya kulipa mshahara kwa mtu asiyefanya kazi; na Mungu amesema asiyefanyakazi asile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa mtumishi mwenyewe binafsi anaweza kuwa na msongo wa mawazo, ulevi na huweza kufa kifo ambacho hakikupangwa na Mwenyezi Mungu. Hilo hilo nalo naomba uliangalie ili teuzi za watu hawa zikikoma basi wapangiwe sehemu za kazi mapema.

Mheshimiwa Spika, lakini kuna watumishi ambao wanatolewa kwenye taasisi kuja kujaza nafasi kwenye Wizara za Serikali na Idara za Serikali, na hapa naomba mpaangalie sana. Watumishi wanaotoka kwenye taasisi wanakuja na mishahara mikubwa, anapofika kwenye Wizara au Idara mwingine ana mashahara kuliko hata Katibu Mkuu wake, sasa sijui hapa kumtuma kunakuwaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili pale kunakuwa na watumishi ambao wameumia na wewe kuanzia vyeo vya chini mpaka wamefika vyeo vya juu. Sasa hao watumishi mnarudisha utendaji kazi wao nyuma. Lakini kama mngekuwa mnawachukua wao mkawapandisha kuwa wakuu wa Idara au wakuu wa Vitengo walio chini yao watafanya kazi vizuri sana ili nao waweze kupanda. Na kwa hili sitaficha, naipongeza taasisi ya Bunge, Bunge wameonesha mfano, Bunge watumishi wao, Wakuu wa Idara, Wakurugenzi, Katibu wao wamezaliwa humo humo kwa watumishi ambao wamewalea wenyewe. Hilo naomba ulichukue tulifanyike kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na niliwahi kuliuliza nikaambiwa vetting sasa huyu tangu akiwa cheo cha kwanza, anaenda mpaka anakuwa principal hizo vetting hazikuonekana? Zinaonekana wakati wa kujaza hiyo nafasi tu? naomba menejimenti ya utumishi wa umma hilo mliangalie.

Mheshimiwa Spika, kuna suala la recategorization, mnakwenda kufanya recategorization; na niliwahi kuuliza swali la msingi nikajibiwa lakini sikuridhika, na kiti cha Spika kikasema swali la Mheshimiwa Janejelly lina logic lakini mmemjibu mnavyoelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupunguza mshahara wa mtumishi ni adhabu kati ya adhabu tatu, lakini sasa huyu mtumishi amesoma watoto wake walikuwa wanakula mlo mmoja ili akajisomeshe anapomaliza anakuja kubadilisha kada mnamwambia tunakushusha na mshahara. Sasa kusoma imekuwa ni adhabu. Lakini niwaambie, hakuna anachokuwa anakwenda kuweka gharama, hata wage bill bajeti yake ni ile ile, nafasi yake mnaweza mkaweka hawa ajira mpya, mkaajiri, ikazibwa naye akabaki na mshahara wake. Mnapopunguza mshahara pension yake mmeipunguza, na kama Mungu ameamua kumchukua mirathi yake mmeipunguza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nishauri kwenye ajira mpya, mnatangaza, wasomi wetu wanaomba wengi, labla nafasi 1000 wameomba 20,000 lakini kwenye usahili ule walioshinda labda ni 1,800 au 2,000. niwambe fungua database, hao 1,000 wape kazi. Sasa, ikitokea mnataka watumishi wengine wa kada ile ile nenda kwenye database peleka hao. Hii itatusaidia kuajiri kwa kufuatana na umalizaji wa vyuo; lakini hii ya kutangaza kila wakati, unakuta aliyemaliza elimu mwaka 2020 anapata ajira wa mwaka 2017 hajapata ajira, nalo naomba mliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ukiyatekeleza hayo utakuwa umetutendea haki watumishi wa Tanzania na tunakuamini haya utafanya. Una kijana hapa anakusaidia, lakini pia wamekupa timu ya watendaji ambayo ninaiamini. Umeletewa Naibu Katibu Mkuu ambaye nimefanya naye kazi, alikuwa boss wangu. Naye haya nilipokuwa nikimwambia alisema sina maamuzi, sasa amepewa maamuzi yupo menejimenti ya utumishi wa umma. Ninawaamini mkiyafanya haya mtakuwa mmemsaidia Mheshimiwa Rais, haya yote anayotaka kufanya kwa watumishi yafanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuna jambo moja ambalo aliwaahidi watumishi, haya aliyaahidi Meimosi na ameyatekeleza lakini aliwaambia nanukuu; “Wanangu la mshahara naomba mnisubiri mwaka ujao wa fedha”.

Mheshimiwa Spika, Ninaamini Mama kauli zake anaziishi kwa hiyo Watumishi wanasubiri Meimosi kuna jambo ambalo litatajwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nguvu za kusimama hapa kuongea, nampongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan hasa kwa masuala aliyoyafanya hapa nchini. Afya, elimu, miundombinu, diplomasia, uchumi lakini mimi nitajilenga kwa aliyofanya kwa watumishi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu ameamua kutoa kwa miaka miwili bilioni 26.3 kwa ajili ya ajira za watumishi nchini, pia akatoa bilioni 23.1 kwa ajili ya kupandisha vyeo Watumishi, zaidi ya hapo akaonesha uungwana wa kutoa msamaha kwa wenzetu waliopata janga la vyeti fake, kuachia bilioni 35.2 ziende kuwalipa hawa watumishi siyo jambo dogo ni jambo kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kwenye hotuba Wizara ya Kazi mmetuambia wamekwishalipa wahanga 11,896. Ni kweli hata mimi nimeenda kwenye Mifuko ya Jamii na Mheshimiwa Waziri nilikupa taarifa. Hata hivyo kuna 541 ambao bado hawajalipwa. Mifuko iliniambia hawajalipwa kwa sababu gani? Taasisi, Wizara na Idara za Serikali hazijapeleka viambatisho vyao na vielelezo vyao ili walipwe, kupitia kiti chako, hizi taasisi ambazo zinajua hazijapeleka vielelezo hivyo zipeleke ili hawa wahanga walipwe basi lengo la Mama Samia litimie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawapongeza mmekuja na electronic ya kuweza kutoa vibali vya ajira na mmefanya, maana mnasema mmetoa vibali vya ajira 8,000 lakini nina imani hivi ni vibali vy ajira vya wageni. Hivi kweli vyuo vyetu vinatoa wahitimu kila mwaka, kelele zetu hapa imekuwa kwamba hatuna ajira nchini, tunatoa ajira 8,000 kwa wageni! Hili tunaandaa bomu na bomu kubwa. Yawezekana Sheria inasema hivyo lakini ilikuwa ni wakati ule hatujapata wasomi wa kutosha. Kama ni Sheria ndiyo inatupeleka kule, basi tukaibadilishe hiyo Sheria ili vijana wetu wanaomaliza vyuo vikuu waweze kupata hizo ajira.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameongelea kaguzi za kiafya za usalama kazini niwapomgeze, lakini mmefanya kwa asilimia 99 na mkapata ambao walikosea 173 na mkawachukulia hatua. Mngefanya kwa asilimia 100 mngepata wengi zaidi. Mimi kuna viwanda ambavyo nimevizungukia kwa Wilaya ya Temeke, kiwanda kile hauwezi kuweka watumishi. Sitovitaja majina lakini ninyi muende mkavizungukie muone. Watumishi wamefungiwa mule, hakuna hewa, hakuna nini, unauliza kisa ni nini? Wataibiwa. Pale kuna maisha ya watu na usalama wa watu, ninawaomba Wizara ya Kazi mkazunguke mfike asilimia 100 mtagundua mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna suala la kisheria la uanzishwaji wa vyama vya wafanyakazi. Kifungu cha (9) cha Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini Na. 6 ya Mwaka 2004, inatoa haki ya wafanyakazi kuunda vyama vya wafanyakazi sehemu zao za kazi na hili ni haki ya Kikatiba. Utaratibu wa kutumia haki hiyo kwa wafanyakazi unasomwa kwenye Sheria Na. 6 ya Mwaka 2004 upo kwenye Kifungu cha 45, ambao unasema sisi tukishaanzisha chama chetu kwa miezi Sita tuna haki ya kuomba kwa Msajili wa Vyama vya Wafanyakazi ili atusajili lakini pale kumekuwa na mgogoro na Mheshimiwa Waziri tumeshaongea mara nyingi na wengine nawazuia wasiende sehemu zingine nawambia tutaongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Waziri ninakushukuru sana nilipopiga simu ulipokea kwa haraka sana lakini ukija kuuliza wanasema vyama vitakuwa vingi, si Sheria mmeitunga nyie kwamba vyama kila mmoja ana hiari wakiwa watu Kumi wanaweza wakaanzisha chama chao sehemu ya Kazi? Majibu yanakuwa vyama vitakuwa vingi sehemu za kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukienda kwenye Halmashauri unakuta kuna TALGWU, CWT na TUGHE sehemu moja ya Kazi. Tunachofanya vyama vikiwa zaidi ya kimoja, viwili, vitatu tunaangalia chenye majority ndicho kinaingia kufunga mkataba kuanzisha Baraza la Wafanyakazi. Kwa hiyo, hii haijakatazwa. Ninashauri tu wale walioomba kawapeni. Hivi mtu anaomba kuanzisha chama chake cha wafanyakazi ninyi mnasema lazima muulize chama kilichopo, nani atakubali kije chama kingine? Hakuna atakayekubali! Sasa mkisema mnawauliza hamtapata lakini mtakuwa mnataka kuibua migogoro ya vyama vya wafanyakazi na kwa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea hapa walipomaliza ukagazi wa afya na usalama, mlitakiwa mtuwekee ukaguzi wa Mabaraza ya Wafanyakazi ambayo sasa hivi yanakaguliwa na CAG lakini sina mahali ninapoona. Ninapozunguka kuna mahali bado Mabaraza ya Wafanyakazi hayafanyiki, na tunajua mabaraza ya wafanyakazi ndilo Bunge la wafanyakazi sehemu ya kazi, ndilo daraja la kujenga mahusianao. Sasa hapa hamjatuonesha kabisa. Sasa niwaombe wakati mnahitimisha mtuambie Mabaraza mangapi yamefanyika? Wangapi hawakufanya kihalali? Pia ni wangapi mmewachukulia hatua kama mlivyosema huku kwenye kukagua usalama na afya kazini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa kwenye asilimia 10 ya Halmashauri. Asilimia 10 ya Halmashauri tumeamua Maafisa Maendeleo ndio wawe wafanyaji wa kuangalia mikopo ile na kuwapa watu mikopo Baraza la Madiwani wakishapitisha. Halmashauri zote nilizozunguka, kilio cha Maafisa Maendeleo wanasema waondolewe hiyo kazi, inawafanya wasitende kazi zao, kwanza wanaifanya bila utaalam. Pili, inawajengea mahusianao yasiyo sahihi kwa chini wakirudi kwenda kufanya kazi yao ambayo ni ya kuelimisha jamii, malezi, mahusiano sasa hawawezi kwenda kwa sababu wakienda wanaenda kudai ile mikopo waliyowapa wale wakopaji, kwa hiyo inawaweka kwenye wakati mgumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifike wakati sasa tuunde vitengo ambavyo vina wataalam, vina Maafisa Mikopo, vinavyo Wahasibu wa kuweza kuwapa hii mikopo. Yawezekana ndiyo maana hizi hela zinapotea, huyu anaetoa hii mikopo hana utaalam wowote wa ktoa hiyo mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri tu kwenye Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Mmefanya mengi sana Mheshimiwa Jenista nakupongeza na najua ambaye amechukua kiatu chako nae ataenda kufanya hivyo lakini kuna tatizo moja la kutokutoa taarifa. Wasaidizi wenu hawatoi taarifa kumbe communication is power! Leo hii Mheshimiwa Rais alikubali kwenye bajeti ijayo hii tunayoijadili sasa iwekwe bajeti ya kufungua barua za promotion za 2016/2017 lakini nilikozunguka kote watumishi hawajui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nawauliza Maafisa Utumishi sasa kama watumishi wenyewe hawajui, rekodi mmezipata wapi za kuwafanyia bajeti hawa ambao walipewa barua zao wakanyang’anywa? Sasa ni jambo zuri Mheshimiwa Rais amefanya lakini hatulitangazi kuonekana ni suala zuri amelifanya likamjengea mahusiano yeye na watumishi. Ninaomba tukafanye hizo nyaraka zisiwe siri, nadhani nyaraka ikishatoka siyo siri. Zamani tulikuwa tunabandikiwa kwenye kuta mnasoma kilichotolewa kwa sababu ikishakuwa wamei – undergrade siyo siri tena lakini unakuta wanakaa nazo kama siri watumishi hawajui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna mikopo ambayo imepelekwa kwenye Manispaa zamani ilikuwa ni kwa Serikali Kuu, mikopo ambayo watumishi hukopeshwa kununua magari (vyombo vya usafiri) lakini hizi Milioni 300 zinazokwenda kwenye Manispaa watumishi hawajui. Unawambia Mheshimiwa Rais na ninyi amewaletea mikopo mkope mnunue vyombo vya usafiri wanaona kama uinawaletea nahau, hawajui! Sasa unamuuliza Mkurugenzi, unawauliza Maafisa Utumishi mnagawaje hizi hela kama Watumishi hawajui? Hizi kawaida yake hufanywa na Kamati inayoingizwa vyama vya wafanyakazi na Wawakilishi kila Idara kuweza kugawiana hizo hela lakini hawajui. Sasa kwa tafsiri iliyopo ina maana zinafika wakubwa wanagawiana wao mikopo, watumishi wa kawaida hawajui.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba hili iende ikafunguliwe. Baada ya hapo naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kupata nafasi hii, leo Mheshimiwa Rais, nimeshamshukuru kwa niaba ya watumishi kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu. Leo niwapongeze Mheshimiwa Simbachawene kwa kuaminiwa kuwa mdau wa Utumishi wa Umma nchini, nikupongeze Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, hongereni sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilivyokuwa naangalia sifa zao wote ni Wanasheria, kwa hiyo kuna makusudi na sababu kuwapeleka Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Waende wakarekebishe sheria, wakaangalie Kanuni na wakaangalie miongozo iliyopitwa na wakati ndani ya utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati nampongeza Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete nilimwambia hivi, kuna sheria ambazo zilitungwa kabla yeye hajazaliwa lakini bado ziko kwenye utumishi wa umma, tumezifanya nazo kama ni imani ya Dini kama ni Biblia na Qurani ambavyo huwa havibadiliki. Niwaombe wakazibadilishe. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, nasema hivyo kwa sababu gani? Kuna standing order inayosema kwenda na nyaraka ya Serikali nje ya ofisi ni makosa, lakini leo hii tunatumiana hata kwenye vishikwambi hizo nyaraka za Serikali. Leo hii tunatumiana kwenye e-mai,l je, ukiambiwa umefanya kosa utatokea wapi? Wakati kuna standing order inayosema hivyo, ndiyo maana ya sheria ninazosema wakaziangalie ni za aina hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nitaongelea ajira kazi kubwa ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma ni ajira, ni kuajiri watumishi ndani nchini, lakini leo TAMISEMI anaajiri, tukikaa Wizara ya Afya itaajiri, hizo ajira tunazi–control vipi? Huko nyuma tulishafanya, Wizara zikapewa mamlaka na idara za Serikali kuajiri. Shida tuliyopata Serikali ikaamua kuunda Sekretarieti ya Ajira na Katibu wake wa kwanza akiwa ni Daudi Xavier ambaye sasa hivi ni Naibu Katibu Mkuu, Utumishi wa Umma, ni kwa sababu waliona haiwezekani, Menejimenti ya Utumishi wa Umma ndiyo iangalie ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya matatizo tunayopata kwamba wameajiri kwa upendeleo wamefanya nini? Ni kwa sababu hakuna ambaye ndiye anayesimamia. Kwa mfano Mama Jenista Mhagama akiwa Waziri wa Utumishi alituambia amefungua kanzidata tukakupongeza, hivi kama hiyo kanzidata ingekuwa inatunzwa na Menejimenti ya Utumishi wa Umma na wao ndiyo wanaajiri, leo hii kulikwa na sababu ya kutangaza kazi hizi tulizotangaza? Tungerudi kwenye kanzidata tukaangalia wale walioomba, nafasi zikawa kidogo wakabaki ndio wangeajiriwa, kwa sababu tayari walikuwa wameshafanya interview. Hii ingepunguza gharama ya Serikali za kurudia tena kwenye kuajiri. Hilo niwaombe Wanasheria wangu wawili hapo wakaliangalie upya, wasimame kwenye instrument yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna miundo inayokinzana, leo hii ukiangalia kwa RAS pale ndiyo anasimamia Halmashauri lakini niongelee kada ya sheria tu iwe mfano. Mwanasheria aliyeko kwa RAS ambaye kazi yake ni kusimamia wanasheria walio kwenye Halmashauri, yeye anaitwa Afisa Mkuu na analipwa mshahara wa kimadaraka lakini wenzake walio kwenye Halmashauri ni Wakuu wa Vitengo na wanalipwa mshahara wa kimadaraka siyo wa kimuundo, huyu analipwa kimuundo hawa kimadaraka. Sasa mtu anayelipwa mshahara wa kimuundo wa Afisa Mkuu atamsimamia ambaye ni Mkuu wa Kitengo analipwa marupurupu yote? Kazi tunaitegemea ipatikane sawa? Ndiyo maana mikataba mingine inapita ya kiajabu ajabu kwa sababu huyu mmeshamdogosha hawezi kumsimamia mtu ambaye anamzidi mshahara na cheo, hilo nalo mkaliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee faragha ya Viongozi. Viongozi wetu tunasema Mawaziri, Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na ninyi Waheshimiwa Wabunge. Kwa nini inaonekana labda viongozi wa sasa hivi hawana maadili mazuri? Ni kwa sababu tumewaondolea haki yao ya faragha. Viongozi wetu, kuwa Waziri Mheshimiwa Jenista hakukutoi kwenye raha zako zingine. Zamani mlikuwa na faragha, mlikuwa na Leaders Club, mlikuwa na Mikoani sehemu za kukaa viongozi wenyewe kwa wenyewe. Kwa hiyo, pale ukikaa hata ukiburudika na bia moja ukadondoka wanakubeba viongozi wenzako na hautalisikia mtaani. Leo hamna pa kukaa mkafanya faragha zenu na hilo limeonekana kama hakuna maadili, lakini maadili ni yale yale, watu ni wale wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaombe Leaders Club ikarudi Menejimenti ya Utumishi wa Umma, hapa Dodoma mjenge Leaders Club ya Viongozi kwenda kupumzika baada ya saa za kazi, na hii inasababisha hata document za Serikali ku- leak. Kwa sababu zamani, ukienda Leaders Club unampelekea Katibu Mkuu document au Waziri aliyepo pemebeni ni Waziri mwenzake au Katibu Mkuu mwenzake, lakini leo tukikuletea Morena kuna simu zingine zina mita 200 zinavuta document unaikuta magazetini. Turudishe hizo faragha.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ndugu zangu niongelee Vyuo vyetu vilivyo chini ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma. Hivi vyuo kila chuo kilianzishwa kwa maana yake. Chuo cha Uhazili Tabora kilikuwa ni kutoa Masekretari mahiri, wenye stenography, leo tunao? Kwa sababu chuo kile sasa tumekibadilisha, kumekuwa na miundo mingi pale, masomo mengi pale kimekuwa ni cha kibiashara. Pia iko wapi IDM Mzumbe ambapo watu walikuwa wakishakuwa Maafisa Wakuu mnapelekwa pale kufundishwa uongozi, kufundishwa uzalendo, kufundishwa maadili. Leo iko wapi? ndiyo maana tunaona maadili hayapo, watu wanateliwa hawajapelekwa mahali popopte kupikwa. IDM imebadilika leo ukitafuta historia yake iliyoianzisha haipo tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Chuo cha Utumishi wa Umma, Magogoni kilikuwa ni chuo cha ku-refresh watumishi waliokazini! Leo hii tumeweka wanafunzi wanaotoka shuleni moja kwa moja, yale maadili yake yameondoka. Niwaombe muende mviangalie vyuo hivyo. Leo hii hatuna wa kuzalisha hata ma-stenographer wa kuja hapa Bungeni wa kwenda Mahakamani wa kwenda kwenye Taasisi za nje zinazokuja hapa. Hawapo hawazalishwi kwa sababu tayari vyuo tumeshavichanganya.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga hoja mkono.(Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nami nashukuru kwa kupata wasaa huu wa kuweza kuchangia kwenye bajeti ya Serikali. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa mambo ambayo anayafanya na maono ambayo ameyaweka mbele ya kugusa kila sekta. Niendelee kumtia moyo na kumwambia asitoke kwenye ujasiri wake kwa kila anachokiamini kwamba kinaenda kuliendeleza Taifa la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na Menejimenti nzima ya Wizara ya Fedha kwa jinsi walivyokuja na bajeti ambayo ni nzuri, inayogusa wananchi wa Tanzania. Pia nampongeza sana Waziri wa Fedha, siyo rahisi mtu kupunguza mipaka yako ya utawala, lakini umekubali kubeba maono ya Mheshimiwa Rais, kujipunguzia mipaka ya utawala, kukubali ile Idara ya Mipango basi irudi kuwa Tume ya Mipango. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa kufurahi kwa sababu ile idara, ile rasilimali iliyo pale na rasilimali watu ya wafanyakzi waliokuwa pale walikuwa hawatumiki ipasavyo. Ni kama walikuwa dormant fulani. Sasa nina hakika wataalamu wataenda kutumika vizuri na kuongeza uchumi wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite kwa mliyofanya kwa watumishi wa Tanzania. Nawapongeza sana, pale Ukurasa wa 36 mmeorodhesha vitu mlivyofanya, lakini naomba niende kushauri sehemu ya madeni au malipo ya watumishi ambayo siyo ya kimshahara. Mmesema mmelipa, lakini naomba mwongeze juhudi, hasa kulipa likizo za walimu, watumishi wa afya walio kwenye Halmashauri zetu Tanzania. Nawapongeza kwa sababu sasa mmeamua stahiki za Wakuu wa Idara zilipwe na Serikali kupitia TAMISEMI. Hilo litaleta heshima iliyo bora kwa wale watumishi na kuongeza hadhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti iliyopita Mheshimiwa Waziri alisimama hapa tukamshangilia sana. Wakaweka posho ya shilingi 100,000 kwa Watendaji wetu wa Kata, lakini posho hii badala ya kujenga, imeenda kubomoa. Watumishi hawa hawalipwi posho hizi ipasavyo. Wengine wanadai mwaka, wengine wanadai miezi mitano; humu nina message nyingi sana, wanasema, Mbunge wetu leo hilo lisemee. Naiomba Serikali, mje na utaratibu mzuri wa kulipa hizo stahili zao ambazo mlikaa hapa zikapotishwa kwenye bajeti ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wastaafu wetu. Kila Mbunge amesimama hapa amesema, kabla mtumishi hajastaafu hupewa barua ya miezi sita kwamba unaenda kustaafu. Sasa kwa nini Serikali msichukue jukumu la kuangalia ni nini kinachodaiwa kwenye mifuko mkakipeleka, kuliko huyu mstaafu sasa? Ameshastaafu na anaanza kuhangaika kufuatilia makato yake, kufuatilia malipo yake kwenye mifuko na wakati ule hana wanaomjua tena Serikalini. Hilo tuliangalie kwa ufasaha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni upande wa elimu. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa bajeti aliyokujanayo iliyoangalia mtoto wa mkulima ambapo sasa vyuo vya ufundi wanaenda kusoma bila ada na vyuo vya kati wanaenda kupata mkopo. Hongereni sana. Pia nashukuru kilichofanyika jana, tumeona kwenye mitandao. Tumeruhusu wanafunzi wa Sudani kuja kumalizia masomo Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa unyenyekevu kabisa nitumie nafasi hii kuiomba Wizara ya Elimu na Serikali, tuna watoto wetu ambao walirudi kwa ajili ya vita kutoka Ukraine. Mpaka sasa hivi hatujafanya utaratibu warudi kwenye vyuo. Leo tumeleta hawa wa nje, hivi hawa wa hapa wanajisikiaje? Naiomba sana Serikali, na Waziri wa Elimu waangalie wazazi waliokuwa na watoto Ukraine ambao wengine ni madaktari, walikuwa wanakuja kuisaidia nchi, wengine ni wahandisi, wengine wanasomea taaluma nyingine mbalimbali, basi nao warudishwe kwenye vyuo wakaendelee na masomo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi sasa kwenye utendaji wa Serikali. Nawapongeza sana, kwani kumekuwa na ushirikiano wa kutosha kwa Mawaziri wetu, mmekuwa wanyenyekevu, tunapowafuata kuuliza tunavyotaka kuuliza, tunapata majibu. Wengine hata tukiwapigia simu saa nane usiku mnapokea. Nawaomba mwendelee na ushurikiano wa aina hiyo, mwendelee kumsaidia Mama, mwendelee kuyakuza maono ambayo yeye ameyaweka mbele, bila kuogopa inasema nini, bila kuogopa miluzi inayopigwa, lakini msimame kwa maslahi ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi tena kwenye afya. Vituo vya afya vimejengwa, lakini nashauri kwamba hakiwezi kuwa kituo cha afya bila wafanyakazi na vitendea kazi. Tunashukuru juhudi za Serikali wameendelea kuajiri, lakini naomba tuwe na mkakati basi kwamba, wakati huu tujikite kuajiri wataalamu wa afya ili vile vituo visije vikageuka magofu. Naomba sana vituo vingi havina wataalam, vituo vingi havina vifaa tiba, basi tuweke nguvu yetu kule tuweze kuendeleza maono ya Mama Samia Suluhu Hassan ambayo ameyaweka mbele maslahi ya Watanzania, ambaye amejitoa usiku kucha akitupigania Watanzania. Basi na sisi tumuunge mkono kwa kuweza kufanya yale maono yake yaonekane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na uzima. Nishukuru pia kwa kupata nafasi ya kuchangia kwa maandishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan - Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa juhudi zake za makusudi kabisa kuwa na utashi wa kupunguza ukali ya bei ya mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Mheshimiwa January Makamba - Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Wakili Msomi Byabato - Naibu Waziri wa Nishati pamoja na watalaam wote wakiongozwa na Katibu Mkuu kwa kazi nzuri mnayoifanya ili kuhakikisha wananchi wanapata umeme. Chapa kazi msigeuke nyuma mkawa mlima wa chumvi, songa mbele na Mungu atawasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirejee kwenye hotuba ya bajeti iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri na kuchangia kwenye vipengele vifuatavyo; kwanza katika hotuba yake ya bajeti Mheshimiwa Waziri ameeleza kuwa gesi asilia sasa itapelekwa nchini Uganda. Niishauri Serikali ihakikishe mikoa ambayo gesi hii inapitia wapate huduma hii ya gesi asilia majumbani kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, faida yake kwanza itafanya wananchi kujiona ni sehemu ya mradi na kuwa walinzi wa bomba hilo lisihujumiwe na itapunguza gharama za matumizi ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu migodi kuunganishwa kwenye gridi ya umeme ya Taifa, migodi hii inatumia umeme mwingi hivyo ni chanzo cha mapato kwa TANESCO. Pia exemption kwenye mafuta Serikali inapoteza fedha nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu matumizi ya gesi asilia kwenye magari na Wizara ya Nishati na Taasisi zilizo chini ya Wizara kutumia gesi asilia, niombe na kushauri litolewe tamko kwa magari yote ya Serikali na Taasisi zote magari yake yatumie gesi ili kubana matumizi ya Serikali kwa kipindi hiki ambacho mafuta yamepanda bei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tungehamasisha matumizi ya gesi asilia kwa wananchi wote, lakini hapa kikwazo ni gharama ya ubadilishaji wa mfumo wa gari kwenda kwenye gesi. Kiasi cha shilingi milioni mbili ni kikubwa mno. Ushauri wangu uangaliwe uwezekano wa kupunguza gharama lakini pia viwekwe vituo vya kutosha vya ubadilishaji mifuko ya magari, kwa kuanzia kila Wilaya ili huduma ipatikane kirahisi wananchi waweze kutumia gesi kwenye magari yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipongeze Shirika letu la TANESCO kwa jinsi linavyobadilika kwa haraka sana. Kwa mimi niliyefanyakazi Wizara ya Nishati ukilinganisha miaka hiyo ya 1990 na sasa ni vitu viwili tofauti kabisa kazi imefanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo cha Shirika kuanzisha Nikonekt App ambayo itarahisisha huduma za kufungiwa umeme kwa Dar es Salaam, Pwani na sasa imezinduliwa Kanda ya Kati na Kanda ya Kaskazini. Hii itaondoa ukiritimba na wateja kupoteza muda ambao ungetumika kufanya shughuli zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa watumishi; watumishi wengi wanafanya kazi kwa mikataba kwa muda mrefu na kwa weledi na uadilifu. Shida na changamoto iliyopo wanapotangaza kazi, hawa hawapewi kipaumbele, wanaajiriwa wapya, matokeo yake na mikataba yao inavunjwa, wanakuwa mitaani, baada ya muda wanafuatwa tena wafanye kama vibarua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili tunapoteza watumishi wenye uzoefu na waliolitumikia shirika kwa uaminifu. Pia tunavunja sheria ya kibarua ambaye hutakiwa kufanya kazi kwa muda wa miezi mitatu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri wasaidie hawa watumishi waliolitumikia shirika kwa muda mrefu, wale wenye sifa wapewe ajira za kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa sababu ndiyo ananipa uwezo wa kusimama hapa leo kuongea.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Mheshimiwa Rais ambaye ndiye Kiongozi wa Chama Cha Mapinduzi kwa kuja na Sera ya kupunguza ada kwa wanafunzi wetu wa form five na form six. Vile vile nampongeza kwa kuangalia maslahi ya watumishi wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara ya Fedha, wamekuja na Bajeti ambayo ni nzuri, bajeti inayogusa wananchi, bajeti ambayo imeangalia kila kona na bajeti ambayo inaenda kuleta maendeleo. Pamoja na kuja na bajeti nzuri nitakuwa na ushauri katika bajeti hii. Nianze na ushauri waliokuja nao wa kupunguza mishahara ya watumishi wale wanaokuwa wamepewa vyeo vya madaraka, kwamba madaraka yanapotoka mshahara wake uondolewe. Hili kwa kweli halitaleta tija bali linaenda kuleta mgogoro kati ya watumishi na Serikali yao. Wanakwenda kumletea mgogoro Mheshimiwa mama Ndalichako na Vyama vya Wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia Sheria ya Utumishi Na.8 kifungu cha 3 kinaongelea mishahara ya mtumishi na haki zake za kimshahara. Ndiyo maana tukihamisha mtumishi kutoka Taasisi, tunajua Taasisi zina mishahara mikubwa, tukimleta Serikalini huwa hatupunguzi mshahara wake, anaendelea na mshahara wake binafsi, lakini kwa hawa wateule tunasema tuwapunguze mishahara. Hapa naomba nishauri kitu cha kufanya, kaumri kangu haka ni Serikali ya Awamu ya Kwanza ndio sijafanya nao kazi, lakini Serikali zilizobaki zote nimefanya nazo kazi. Zamani uteuzi wa District Executive Directors, District Administrative Secretaries na Regional Administrative Secretaries, uteuzi wote walikuwa wanaenda kwa watumishi ambao wameshakomaa ndani ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, mtumishi alikuwa akifika cheo cha Muundo cha mwisho Principal Serikalini, mnaanza kumtania kwamba wewe subiri mwenye mamlaka akuone, kwa sababu hawezi kwenda popote na huyu ameiva kabisa, lakini tuangalie sasa hivi tunawatumia? Hatuwatumii. Kwa hiyo unakuta mtu anaweza akateuliwa kuwa DED au DAS amemaliza Chuo Kikuu tu, hajapata uzoefu ndani ya Serikali, huyu akienda lazima mambo hayatakwenda vizuri na huyu akirudi sasa ndiyo hawa Wakurugenzi Mheshimiwa Waziri ametaja kwamba tunao 300, wamekuja kwa muundo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zamani hawa wateule, walikuwa wanachujwa na Menejimenti ya Utumishi wa Umma, ndiyo kazi yake kuchuja hawa wateule na walikuwa wakienda wanafanya kazi kwelikweli, lakini hawa tunaopeleka sasa hivi watu wamekuwa wateule wa Mheshimiwa Rais. Unakuta DC anamwambia DED mimi ni mteule wa Rais, DED naye anamwambia mimi ni mteule wa Rais, kazi zinaanza kushindwa kwenda hapa. Sasa ili waweke vizuri lazima mmoja atapigwa chini, sasa huyu anayepigwa anaongeza idadi hiyo ambayo Mheshimiwa Waziri amekuja nayo.

Mheshimiwa Spika, sasa leo tunasema tuanze kuwashusha mishahara, kushusha mshahara mtumishi inatakiwa uunde Tume, umfungulie mashtaka, Tume ije na majibu kusema anatakiwa kati ya adhabu tatu apate mojawapo. Moja huwa ni kushushwa cheo ambayo mmeshampa sasa, mmepiga chini; pili ni kupunguziwa mshahara na tatu ni kufukuzwa kazi. Sasa hizi adhabu tunazoenda kuwapa za kuwapunguzia mishahara Tume gani tumeunda ikakwambia huyu anafaa kupunguziwa mshahara. Hapa naomba Serikali iliangalie kwa mapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara imesema viongozi wakopeshwe magari, nakubaliana nalo kabisa, lakini tunaweza tukaenda kupoteza viongozi. Awamu ya Tatu ilijaribu wakakopeshwa magari lakini tulipata ajali nyingi sana za viongozi. Anatoka Ofisini amechoka anajiendesha kurudi nyumbani anagonga, saa zingine anawaza Mkuu wake wa Kazi kashampa mikakati ya ajabu, ataifanyaje mwisho wanagonga magari. Tuliwahi kumpoteza Kamishna mmoja alikuwa Kamishna wa Madini, kwa ajali ya kutoka usiku kazini, tuliangalie nalo kwa mapana.

Mheshimiwa Spika, pia imesema CAG wanamwongezea nguvu. Twende tuangalie hayo matumizi, tuwabane kwenye matumizi, tuwabane kwenye manunuzi, ndiko kunakoharibu fedha nyingi ya Serikali, lakini siyo kusema kwamba tuwape magari, tuliwapa halafu baadaye tukaendela kuwapa magari ya Serikali, hapo sioni kama tutaweza kwenda napo vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishauri kwenye ukusanyaji wa mapato. Tumeangalia tu ukusanyaji wa mapato, lakini tumejisahau kwenye maduhuli ya Serikali na haya ndiyo makubwa zaidi na hapo ndipo tunapopoteza mapato. Maafisa Masuuli wetu wamepewa mamlaka ya kusimamia matumizi, lakini kwenye mapato wanapasahau. Sasa sijui utasimamiaje matumizi kama hutafuti hayo mapato ili uje kuyatumia. Niishauri Serikali tu Mlipaji Mkuu wa Serikali aingie mikataba na Maafisa Masuuli ya kukusanya maduhuli, asipofikia kiwango cha kukusanya, basi matumizi wasimpe, kwa sababu hakusanyi anachotaka kuja kutumia na mianya inayoleta maduhuli haya yasikusanywe ipo mingi.

Mheshimiwa Spika, twende kwenye pass za kusafiria, passport ambayo ni haki ya kila Mtanzania kuipata nchini humu, angalia utaratibu wake wa kuitafuta, unajaza mafomu, ukijaza ukifika Uhamiaji kwenye counter pale, unakutana na Maafisa wanakwambia hii font uliyotumia, mjazo uliojaza siyo wa kiuhamiaji, rudi ukaanze upya, lakini wanakuelekeza nenda hapo nje. Ukienda Kurasini pale nje, stationery zipo kama uyoga, Ofisi za Wanasheria zipo kibao, unaenda kuanza upya. Sasa kuanza upya kama huyu raia hana safari anarudi nyumbani anaachana navyo kwa sababu alishapanga Sh.20,000 ya Mwanasheria mara ya kwanza amelipa imeharibika, kulipa tena hawezi na muda wake unapotea.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa napiga hesabu kidogo tu ya kujumlisha na kutoa, Watanzania 2,000,000 wakirudi nyumbani bila kuendelea na pass hizo 50 mara 2,000,000 tunapoteza bilioni 100 hapo za maduhuli zinaondoka, lakini sasa aliyepenyeza akapata hiyo passport ikiisha, akirudi anaanza utaratibu uleule wa usumbufu, lakini hii si ni elektroniki, ukiweka kitambulisho changu cha NIDA si unaona rekodi zangu zote. TRA wanawezaje, mbona ukienda leseni imeisha, wakiweka ile leseni, wanatoa wanakuona rekodi zako, unalipa 70,000 wanakupa leseni yako mpya unaondoka. Huku kwenye passport tunashindwaje, kuweka ile NIDA tukaona rekodi za huyo raia, tukampa pass yake ya kusafiria. Kwa hiyo sasa pass imebaki siyo Sheria ya Kikatiba kwamba tuna haki ya kumiliki pass za kusafiria, imebakia unaitafuta wakati unataka kusafiri. Hapa ukitupa safari ndiyo tutahangaika kutafuta pass kwa sababu unaona unahangaika bure, hapo tunapoteza mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuje NIDA, NIDA napo kuna mapato yanapotea kwa kuzungusha raia kupata vitambulisho vya NIDA na penyewe ukichukua tu watu 2,000,000 waone huu usumbufu waache waende pembeni, kwa 20,000 tunapoteza bilioni 40, hapo ni kwenye NIDA napo pia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, niongeze dakika mbili tu nimalizie.

SPIKA: Mbili utakuwa unampunguzia mwenzako mwenye muda wake, sekunde 30 malizia sentensi.

MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Twende kwenye NIKONEKT ya TANESCO waliyoanzisha, si rafiki kwa raia. Napeleka kadi ya NIDA wanaweka namba, lakini ile fomu ina maswali, inakuuliza mpaka babu wa bibi yako. Babu wa bibi yako nani? Jina lako nani? Shule ya msingi umesoma wapi? Wakiweka namba za NIDA si wanaona hivyo vitu. Naomba wafanye hii mitandao yote isomane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga hoja mkono, ahsante sana. (Makofi)