Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Zuena Athumani Bushiri (1 total)

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na changamoto nyingi sana katika Taifa letu za ucheleweshaji wa kesi Mahakamani jambo ambalo linasababisha huduma ya utoaji wa hukumu kuchelewa. Je, Serikali ina mpango gani katika kuongeza huduma za mobile za Mahakama ili kuisaidia Serikali au nchi kwa ujumla kupata huduma za Mahakama kwa muda mfupi kwa maana ya kwamba kesi ziweze kumalizika kwa kupitia Mahakama za mobile. Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba muhimili wa Mahakama umetafuta njia nzuri ya kupunguza kesi au kuondoa mlundikano wa kesi kwenye kesi zilizopo nchini. Idadi ya makosa imekuwa kubwa na sasa Mahakama zetu hazitoshi kwa sababu nyingine, matatizo mengine yanatoka kwenye vijiji ambako pia hakuna huduma ya Mahakama.

Nini muhimili wa Mahakama umefanya ni kutafuta njia nyingine rahisi zaidi ya magari yanayobeba banda litakalotoa huduma za Mahakama (mobile court) kama ambavyo Mbunge amesema.

Mheshimiwa Spika, huduma hii tumeshaanza kuona kuwa unatija, kwamba magari yale yanasafiri mpaka vijiji ambako wananchi wenye uhitaji wapo ili utoaji haki ufanyike hukohuko vijijini bila wananchi hao kulipa gharama kubwa ya nauli kwenda kufuata Mahakama ya mwanzo ambazo ziko nyingi kwenye ngazi ya Tarafa au Mahakama ya Wilaya pekee. Kwa hiyo Muhimuli wa Mahakama kupitia mpango wake na Wizara ya Katiba na Sheria itakapokuja hapa itatueleza, kuongeza mobile court, au magari haya mengi yasambazwe kwenye maeneo yetu yote kwenye Wilaya ili yaweze kuwafuata wananchi kuweza kupunguza mlundikano wa kesi uliopo kwa lengo lile lile la kutoa haki kwa wale wote wanaohitaji matatizo yao kusikilizwa na Mahakama zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nichukue wazo hilo na Waziri wa Katiba na Sheria yuko hapa alichukue hilo walifanyie mkakati naamini kwenye bajeti yao lipo niwasihi Waheshimiwa Wabunge tupitishe bajeti ya Katiba na Sheria ili sasa waweze kununua mobile court nyingi ziende kwenye vijiji vyetu na maeneo yetu na wananchi waweze kupata huduma, ahsante sana. (Makofi)