Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Zuena Athumani Bushiri (15 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa Bungeni, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa kibali hiki kwa siku hii ya leo na niwashukuru wapiga kura wangu wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro kwa kunichagua kuingia katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niko katika ukurasa wa 34 wa hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa tarehe 13 Novemba, 2020. Kwanza niipongeze Serikali kwa kutekeleza miradi mikubwa ya maji, 1,423. Hii ni katika sera ya kumtua mwanamke ndoo ya maji. Katika Mkoa wa Kilimanjaro, tunazo wilaya ambazo zina matatizo ya maji na wilaya hizo ni Wilaya ya Mwanga, Same pamoja na Wilaya ya Rombo. Wilaya hizi mbili zimetolewa majibu na Waziri wa Maji asubuhi na bahati Mbunge wa Jimbo la Same aliongozana pamoja na Waziri wa Maji kwenda kuongea zaidi kuhusu mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kuhusu Mradi wa Maji wa Ziwa Chala ambao ni mradi mkubwa ambao uko katika mipango ya kutekeleza katika Wilaya ya Rombo. Wilaya ya Rombo ina changamoto kubwa sana ya maji, mwanamke anaweza akatoka asubuhi nyumbani kwake, akatumia masaa sita kwenda kutafuta ndoo moja ya maji. Katika kutatua suala hili la maji, kuna mradi mkubwa ambao unatekelezwa katika Wilaya ya Rombo, Mradi wa Ziwa Chala, lakini mradi huu hauna fedha za kutosha. Hivyo, niiombe Serikali iwasaidie akinamama hawa, akinamama ambao wameifanya kazi kubwa sana katika uchaguzi huu kuhakikisha kwamba Chama Cha Mapinduzi kinaongoza Wilaya ile ya Rombo. Tuiombe Serikali ifanye haraka ili mradi huu ukamilike ili tuwatue akinamama ndoo ya maji katika Wilaya ya Rombo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichangie katika ukurasa wa 19 kuhusu sekta ya viwanda, Manispaa ya Moshi Mjini ina viwanda vingi ambavyo vimefungwa amejaribu kuchangia Mbunge wa Jimbo, lakini kama mkazi wa manispaa ile na kama mwanamke ambaye naiangalia Serikali ya chama changu kwamba inao uwezo wa kufufua viwanda vile. Viwanda vile vimefungwa kwa muda mrefu na ni viwanda vingi ambavyo vimekosesha ajira kwa vijana, akinamama na wananchi wa Moshi kwa ujumla. Tuiombe Serikali sasa iwasaidie Manispaa ya Moshi, angalau ajira ziweze kupatikana, viwanda hivyo viweze kufunguliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi katika Wizara ya Afya, kwanza niipongeze Serikali kwa kujenga vituo vya afya pamoja na hospitali za wilaya, lakini wilaya zetu hizo zinakuwa bado hazina dawa za kutosha. Tuiombe Serikali na Wizara ya Afya ijaribu kufuatilia na kupeleka dawa katika hospitali zetu za wilaya na vituo vya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nyongeza ya hiyo, kuna changamoto katika Wizara ya Afya, kuna huduma ya mama na mtoto, huduma hii katika maeneo machache ya vijiji watumishi wetu wamekuwa sio waadilifu, kwa kuwa tunavyotambua kwamba huduma hii ya mama na mtoto chini ya miaka mitano inatolewa bure.

Hata hivyo, baadhi ya watumishi wetu wanakuwa wakiwatoza akinamama hata wanapopeleka watoto wao kliniki na hata wanapoenda katika masuala ya kupima uzito tunaiomba Wizara ya Afya, ifuatilie ili iweze kubaini watu hao, watendaji hao ambao wanaichonganisha Serikali yao na wananchi kwa kuwa Serikali inatambua kwamba huduma hii inatolewa bure, wananchi wanakuwa wanajenga chuki na Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niunge mkono hoja ya hotuba ya Mheshimiwa Rais. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, nianze kuipongeza Serikali ya CCM kwa kazi kubwa na nzuri inayofanywa katika sekta ya elimu, pia nampongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa jitihada kubwa anazozifanya kwenye sekta ya elimu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga madarasa mengi sana nchi nzima na kwa mara ya kwanza Tanzania imebadilisha historia kwa wanafunzi wote waliofaulu kupata nafasi ya kuingia kidato cha kwanza. Ongezeko la madarasa haya imeongeza idadi ya upungufu wa walimu. Naishauri Serikali iongeze ajira za walimu ili idadi ya madarasa iendane na idadi ya walimu.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ni shule za zamani kuwa na uchakavu mkubwa, naishauri Serikali pia ifanye ukarabati wa shule hizo kongwe ili ziendane na shule mpya zilizojengwa sasa hivi. Sambamba na hilo ipo changamoto ya walimu kukosa nyumba karibu na shule wanazofundishia, niendelee kuishauri Serikali ijenge nyumba za walimu kupunguza changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, niongelee kuhusu mitaala yetu ya elimu, nashauri Serikali kuwa mitaala yetu iendane na mafunzo ya ufundi iwe kuanzia darasa la kwanza kumwezesha mwanafunzi anapomaliza shule awe anaajirika na awe na uwezo wa kufanya kazi na awe anaweza kujiajiri.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ili nami nichangie kuhusu hotuba ya bajeti ya Waziri Mkuu 2021/2022. Mimi nitajikita zaidi katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri na kazi ambazo amezifanya katika Taifa hili la Tanzania. Pia niipongeze Serikali kwa kujenga na kuimarisha miundombinu ya afya katika nchi nzima ya Tanzania. Pia niipongeze Serikali kwa kutoa dawa na vifaa tiba katika maeneo mengi ya zahanati zetu pamoja na hospitali zetu nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mipango mizuri ya Serikali tumeweza kujenga miundombinu mingi katika nchi yetu. Kwa mfano, tumepata vituo vya afya vya kutosha, zahanati za kutosha na hospitali za rufaa nyingi nchini Tanzania. Hata hivyo, kila lenye mafanikio lazima tukubali kuwa litakuwa na changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika zahanati hizi ambazo zimejengwa zimekuwa na uhaba wa madaktari pamoja na wauguzi. Utakuta maeneo mengine hasa maeneo ya vijijini zahanati moja inahudumiwa na daktari mmoja wakati wanaoitumia ni zaidi ya vijiji viwili au vitatu. Niiombe Serikali sasa ione umuhimu wa kuongeza bajeti katika sekta hii ili zahanati na hospitali zetu ziweze kupata watumishi stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna upungufu wa dawa. Nadhani Wabunge wenzangu wote wanakiri kwamba hospitali zetu zimebakia madaktari kwa professional zao ambazo wakishakuandikia dawa unaenda kutafuta hela ili ukanunue wewe mwenyewe, maeneo mengi dawa hazipatikani. Niiombe sasa au niishauri Serikali iweze kuongeza bajeti katika sehemu hii ambapo dawa zinahitajika sana ili wananchi wetu waweze kupata haki stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunajua kwamba ugonjwa wa COVID-19 umetingisha sana nchi yetu, kumekuwa na upungufu wa mitungi ya gesi. Wananchi wengi wanaoishi vijijini wanaopata magonjwa yale wanakosa oxygen na hivyo kuhatarisha maisha yao kwa sababu unapotaka kupata mitungi ya oxygen ni lazima uende katika hospitali kubwa za mikoa, halmashauri au rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali sasa, ili kuwasaidia wale wananchi ambao wapo vijijini, Serikali itenge fedha za kutosha ili iweze kupeleka mitungi hii hata katika ngazi ya zahanati ili kuokoa wananchi wetu walioko vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa sijatendea haki wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro kama nitakuwa sijachangia hospitali ya Rufaa ya Mawenzi katika Jengo la Mama na Mtoto. Hospitali ya Mawenzi ina jengo la Mama na Mtoto ambalo limejengwa tangu 2008. Ni takribani miaka 13 sasa jengo hilo halimaliziki. Hospitali ya Mawenzi inatibu wilaya saba za Mkoa wa Kilimanjaro. Kwa hiyo, ukienda katika wodi ya zamani ambayo pia ni chakavu kwa majengo, unakuta wanawake wanalala wawili wawili; mmoja anageuzia kichwa huku na mwingine kule na vitoto vyao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba katika hili Serikali iweze kutenga fedha ili iweze kumalizia jengo lile na wanawake waweze kujifungua salama na katika maeneo ambayo ni mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, nami naomba kuchangia hotuba ya Wizara ya Maji na nianze kwa kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kupitia Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya kuhakikisha anamtua mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika Wakala wa Maji Safi na Mazingira Vijijini (RUWASA); niongelee tatizo la maji katika Wilaya ya Same Jimbo la Same Mashariki katika Vijiji vya Maore, Kadando na Muheza. Vijiji hivi vimekuwa na tatizo la maji kwa muda mrefu sasa baada ya intake kusombwa na mafuriko ya mvua yaliyotokea Desemba, 2021. Mradi huu wa maji ulijengwa tangu mwaka 1967 idadi ya watu ikiwa ndogo sana, hivi sasa idadi ya watu imeongezeka sana.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ipeleke pesa za ujenzi wa intake na kukarabati miundombinu ambayo imekuwa chakavu kutokana na muda mrefu tangu ilivyojengwa.

Mheshimiwa Spika, nichangie pia kuhusu uchimbaji wa visima nchini. Maji ni uhai; kutokana na kauli hiyo niipongeze Serikali kwa kuchimba visima vya maji kwa maeneo ambayo hayana vyanzo vya maji. Ni naishauri Serikali iongeze bajeti katika eneo hili la uchimbaji wa visima ili kupunguza changamoto ya maji na kuwafanya wanawake wafanye kazi za uzalishaji badala ya kutumia muda mwingi katika kutafuta maji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi kuchangia hotuba hii ya bajeti ya Mawasiliano, Teknolojia na Habari. Tunatambua kwamba, Habari na mawasililiano ni kila kitu. Bila mawasiliano hakuna biashara, bila mawasiliano hakuna kazi, bila mawasiliano hakuna kitu chochote kinachoweza kuendelea katika Mataifa yaliyoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasimama hapa kwa masikitiko makubwa sana kwamba katika Mkoa wa Kilimanjaro kuna baadhi ya Kata ambazo ziko kwenye mipaka ya mikoa ambazo hazina mawasiliano kabisa. Kenya Safaricom imekuwa ikitawala maeneo ya mipakani kwa sababu wananchi wa maeneo hayo hawapati mawasiliano ya nchi yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2021 nilisimama katika Bunge hili nikaongelea maeneo ambayo yameathirika sana ikiwepo Wilaya ya Rombo, maeneo yote ya mpakani; Wilaya ya Mwanga, Kata za Kivisini, Jipe, Kigonigoni, Kwakoa na Toloha. Nasikitika kwamba maeneo haya kwanza yana hatari ya wanyama wakali, lakini pamoja na hatari hiyo hawana mawasiliano kabisa, hawawezi hata kujikwamua katika shida wanazozipata kuwasiliana ili wapate misaada. Naiomba Serikali iangalie maeneo yale ambayo ni hatari kwa wananchi ipeleke minara ile ili wananchi wakapate huduma stahiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisimama tena hapa mwaka 2021 nikiongea Habari ya minara katika Hifadhi ya Mkomazi. Hifadhi ile inapita barabara ambayo inaenda katika Makao Makuu ya Wilaya ya Same ambayo inategemea Vijiji vya Ndungu, Maore, Kihurio, Kisiwani, Kadando, Mpirani na vingine vingi vya maeneo ya milimani; wanategemea kupita barabara ile kwenda Makao Makuu ya Wilaya. Pamoja na hayo, wafanyabiashara wengi wa maeneo hayo wanaenda kufungasha mali zao Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pametokea na changamoto ya vijana kuvamia maeneo hayo na kuvamia baadhi ya Land Rover zinayopita pale kuiba na kupora mali za wananchi. Naiomba Serikali yangu Sikivu iangalie wananchi wake taabu wanazopata ili ione umuhimu wa kupeleka minara eneo lile ili wananchi wa maeneo yale wapate huduma stahiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ikumbukwe kwamba hifadhi ile sasa hivi imekuwa na wanyama wengi sana. Tembo kama tunavyosikia na tunavyoendelea kusema kwamba, tembo wamekuwa ni changamoto kubwa sana. Eneo lile zamani nikiwa mtoto, kwa kuwa ndiko nilikozaliwa, lilikuwa linaitwa kambi ya simba. Kwa hiyo, lina wanyama hatarishi. Inawezekana wananchi wakapata matatizo katika eneo la hifadhi, lakini wanashindwa kujikwamua pa kupata msaada. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali, wakati mtakapokuja kuhitimisha hapa leo, mimi sitashika Shilingi, lakini mtuambie ni lini mtapeleka minara katika maeneo ya mipakani ili wananchi wale nao wakapate huduma stahiki? La kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini pia mtapeleka minara katika maeneo ya hifadhi ya Mkomazi Game Reserve ili wananchi nao wakaweze kupata huduma stahiki? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kukushukuru kunipa nafasi hii kuchangia katika Wizara ya Kilimo. Nianze kwa kuwapongeza Waziri wa Wizara ya Kilimo, Naibu Waziri na Watendaji wake wote kwa kazi nzuri sana wanazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza katika kilimo cha umwagiliaji, umwagiliaji wa mpunga pamoja na tangawizi. Kilimo cha mpunga ni kilimo cha chakula na biashara, kilimo cha mpunga kinaingizia kipato sana wafanyabiashara, kilimo cha mpunga ni kilimo ambacho kinahitaji maji ya kutosha, lakini kwa tabia ya nchi mvua zimekuwa chache sana hivyo mazao ya kilimo cha mpunga yamekuwa machache sana.

Mheshimiwa Spika, natambua kwamba Serikali imejipanga mipango mizuri sana ya kuweza kuwezesha kuweka miundombinu endelevu katika sekta ya umwagiliaji. Nitoe mfano katika kilimo cha umwagiliaji wa mpunga katika Lower Irrigation Moshi, Lower Irrigation Moshi ilianza na hekta 2300 lakini hadi sasa hivi zinalimwa hekta 1100 hii inatokana na miundombinu chakavu ambayo imejengwa tangu mwaka 1987. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kweli Serikali nia yetu ni kuboresha miundombinu hii katika skimu zetu ni vizuri tukaelekeza nguvu ili tuweze kufanyakazi ya kusaidia wakulima wale ambao wametengeneza mabwawa yao ili Serikali iongeze nguvu ya kutengeneza mabwawa ya kutosha ili kilimo cha umwagiliaji kiwe kilimo endelevu.

Mheshimiwa Spika, nije katika suala zima la kilimo cha tangawizi, wote tunatambua kwamba kwa kipindi hiki cha Corona tangawizi imekuwa ni kilimo ambacho kimeleta tija sana nje na ndani ya Tanzania, hakuna familia ambayo inaweza ikalala bila kukosa kipande cha tangawizi. Kule Same Mashariki katika Mkoa wa Kilimanjaro wilaya ambayo inalima sana zao hili la Tangawizi, wakulima wamekuwa wakilima kilimo hiki kwa shida sana kwa sababu ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kilimo cha tangawizi kinahitaji maji ya kutosha, wamejaribu kujisukuma wao wenyewe na kutengeneza miundombinu ya maji kwa maana ya kutengeneza mabwawa Wapare wanaita ndiva. Ndiva ni mabwawa madogo.

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali ili kusaidia kilimo hiki kiweze kukua iweze kusaidia wakulima wale kuwatengenezea mabwawa ambayo yatavuna maji kipindi cha mvua ili kilimo hiki cha tangawizi kiwe kilimo endelevu na kiweze kuwaingizia mapato wakulima wetu pamoja na Serikali kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, nije katika zao la vitunguu, zao la vitunguu linalimwa mkoani Kilimanjaro ni biashara kubwa sana kwa akina mama kule Kilimanjaro ukienda utakuta akina mama wamebeba makarai wanauza vitunguu, vitunguu vinalimwa Himo, vitunguu vinalimwa Hai, vitunguu vinalimwa Ruvu, vitunguu vinalimwa katika Kijiji cha Gonja, Mahore, Mpirani, Kalung’oyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakulima wanatumia nguvu nyingi sana katika kilimo hiki, lakini nguvu zao zote zinaishia pale ambapo maji yanakuwa hayapatikani ya kutosha. Bado niendelee kuiomba Serikali ili kilimo hiki kiweze kushamiri na kuwapatia mapato wananchi. Naomba iendelee, hoja yangu iendelee ile ile ya kuomba Serikali itengeneze mabwawa, na kilimo hiki kimeleta manufaa sana kule Kilimanjaro kwa sababu vitunguu vingi vinauzwa Kenya, soko la Himo ndipo wafanyabiashara wanaotoka Kenya wanapovuka pale na kununua vitunguu hivi, kwa hiyo, ni zao ambalo linawaingizia mapato. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Zuena Bushiri.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kunipa nafasi nichangie bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayofanywa katika sekta hii ya barabara nchi nzima. Pia nataka niwapongeze waziri Naibu Waziri na watendaji wote wa wizara hii, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sikumpongeza Meneja wangu wa TANROADS wa Mkoa wa Kilimanjaro, Eng. Mota Kyando Mama ambaye anafuatilia sana barabara za Mkoa wa Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende katika mchango wangu ambao nitachangia barabara mbili katika Mkoa wa Kilimanjaro. Barabara ya kwanza ni barabara ya Tarakea Holili ambayo ina Km 53. barabara hii imetengewa Shilingi Bilioni 5.8 ninaishukuru Serikali, lakini barabara hii ina urefu wa KM 53 kwa maana ya kwamba hela iliyotengwa haitoshi, ninaiomba Serikali iongeze fedha ili barabara hii iweze kukamilika kwa kiwango cha lami. Kwa kuwa barabara hii ni barabara ambayo iko katika mpaka wa Kenya na Tanzania, ni barabara ambayo ina unganisha border mbili barabara hii inaunganisha border ya Tarakea kwenda katika border ya Holili, hii ni barabara ambayo inaongeza uchumi wa nchi na wananchi wa Rombo kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Rombo wanategemea kilimo na biashara hasa akina mama, wanategemea barabara kwa ajili ya kuvusha biashara zao, kule Rombo bila barabara watu wanashindwa kupeleka mazao yao katika masoko, ninaiomba Serikali iongeze bajeti hii hili barabara hii iweze kukamilika kwa kiwango cha lami, pia ikumbukwe kwamba barabara hii ni muhimu kwa ajili ya ulinzi na usalama katika mpaka wetu wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuongelea barabara hii niongelee barabara nyingine ya Elerai - Kamwanga ambayo ina Km. 44. Ninaishukuru pia Serikali kwamba imetutengea Bilioni Mbili katika barabara hii, lakini nirudie kwamba Bilioni Mbili hazitoshi katika barabara ile, barabara ile inatumika sana kwa kupitisha watalii, wanaotoka KIA wakipitia Bomang’ombe kuja Sanyajuu, Kamwanga na kuingia katika Wilaya ya Rombo, kwa hiyo barabara hii inaunganisha Wilaya ya Rombo na Wilaya ya Siha.

Mheshimiwa Spika, wakina Mama wa Siha hawatofautiani na akina mama wa Rombo ni akina mama ambao wanajitafutia riziki kwa kupitia biashara ya viazi, hivi viazi vya chips tunavyokula huku vinatoka vingine Siha na kule Rombo ninaomba Serikali itengeneze barabara hii, kwanza kuinua uchumi wa maeneo haya Wilaya hizi, lakini pia ikumbukwe kwamba watalii watakuwa wanazunguka ule mlima kutoka Wilaya ya Siha kuingia Rombo na kuingia katika mpaka wa Holili au Tarakea.

Mheshimiwa Spika, mimi sina mengi niishukuru Serikali lakini naendelea kulilia Serikali iongeze hela hizi ili hizi barabara ziweze kukamilika kwa kiwango cha lami. Baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza Rais wetu, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kuibadilisha historia ya Tanzania kwa kuwa Rais wa kwanza Mwanamke katika nchi yetu, pia nimpongeze Mama yetu kwa kutuletea bajeti ya kihistoria, bajeti ya mwanamke katika Taifa letu la Tanzania. Kule Kilimanjaro wanasema bajeti hii ina mshiko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niwapongeze Mawaziri, nimpongeze Waziri wa Fedha, Naibu Waziri na Watendaji wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi nianze kuchangia katika Sekta ya Nishati. Nimpongeze Rais wetu kwa kusikiliza kilio cha Watanzania wengi ambao Wawakilishi wao ambao ni Wabunge wakaja kulia kilio hiki katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusu suala la zima la umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali kwa kutoa tozo la nguzo la umeme kuanzia shilingi 327,000 hadi 27,000, Tanzania bila giza inawezekana. Wote tunaelewa kwamba umeme ndiyo chachu ya maendeleo, Tanzania bila umeme hakuna Tanzania ya Viwanda, vijana wetu wengi wamefanya kazi nyingi sana katika nchi hii lakini mara nyingi sana wamekuwa wakikimbilia mijini kwenda kutafuta ajira. Baada ya Sera ya umeme vijijini vijana wengi wamepata ajira katika vijiji, wamejiajiri na hata wengine wameajiri wenzao tuipongeze Serikali katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia, tunao wanawake wengi ambao wanajishirikisha katika biashara za mama lishe, wanawake hawa nao wamefaidi umeme vijijini kwa kuwa wameweza kutengeneza mazingira ya kuboresha biashara zao kama vile kutengeneza juisi na hata kuwa na friji kwa ajili ya kuhifadhi vyakula vyao. Niipongeze sana Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuipongeza Serikali kupitia nishati nije suala zima la Madiwani. Wote tunatambua kwamba Madiwani wana kazi nyingi sana katika Kata zao nani wawakilishi wetu ambao wanafanya kazi nyingi sana katika maeneo yao. Niipongeze Serikali kupitia Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kusikiliza kilio cha Madiwani ambao sasa fedha zao zitakuwa zinatoka Serikali Kuu badala ya Halmashauri zao. Hii itawaletea nguvu sana kwa kuwa watakuwa wanapata fedha zao kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi niiombe Serikali yangu sikivu tunatambua kazi nyingi wanazozifanya Madiwani katika maeneo yao ikitokea misiba wataombwa majeneza, ikitokea shughuli wataombwa hiki na kile, kukiwa na wagonjwa wataombwa usafiri ni hela hizi hizi, posho hii hii ambayo ndiyo wanayoitumia. Niiombe Serikali yako sikivu iwaongezee posho Madiwani hawa, naungana na wenzangu wote waliochangia hili kwamba ni vizuri Serikali ikawatazama sasa na wao waweze kuongezewa posho ili angalau waweze kuendesha shughuli zao vizuri na kwa amani katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije suala la TARURA, niipongeze Serikali Wabunge wengi sana hasa wa Majimbo wamekuwa wakilia kilio cha TARURA humu ndani tukiwepo na sisi wanawake wa Viti Maalum. Wengi wameongea mengi kuhusu suala la barabara, bila barabara hakuna maendeleo, wakulima kilimo kinahitaji barabara, wananchi wenyewe tunahitaji barabara, wameongea wengi wakasema kwamba hata akina mama wengine wakati wakijifungua wanajifungulia njiani kwa sababu ya barabara zetu kuwa mbovu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, uongozi wa mwanamke siku zote mwanamke huwa anaangalia mtoto analia nini, mama ameweza kuangalia nini watanzania wanacholilia akajaribu kuleta bajeti hii katika Bunge hili ambalo kila Mbunge amefurahia bajeti hii na kwa kupitia Bunge hili Watanzania wengi kila mtu amefarijika na bajeti hii. Niseme kwamba tozo kwa ajili ya barabara ya TARURA ambayo zaidi ya shilingi milioni 222 zikipatikana nakutekeleza malengo kama ilivyokusudiwa naamini kwamba 2021/2022 ifikapo mwishoni tutakuwa barabara zetu zote zinapitika kipindi chote cha mwaka. Niiombe Serikali ipeleke pesa hizi zikafanye kazi iliyokusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo mimi niunge mkono hoja. Nasema ahsante sana kwa bajeti hii nzuri. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inavyoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan; nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote.

Mheshimiwa Spika, nianze kuchangia kuhusu wanawake wanaovyonyanyasika kwa kutelekezwa na waume wao; kumekuwa na tabia ya wanaume kutelekeza wake zao na watoto na kusababisha watoto kukosa haki zao za msingi kama elimu, chakula, malazi na mapenzi ya wazazi wao wote. Wanawake wanaotelekezwa kwanza wanaathirika kisaikolojia na kusababisha hata kukosa malezi bora. Niishauri Serikali kutunga sheria kali ili kudhibiti hali hii.

Mheshimiwa Spika, nichangie pia kuhusu suala la nyumba za kulelea wazee nchini. Tunao wazee wengi sana ombaomba ambao hawana uwezo katika Taifa letu, wazee hawa wengine hawana nyumba bora za kuishi wengine hawana chakula, nguo na kadhalika. Niiombe Serikali kwanza ihakikishe kila mkoa kunakuwa na nyumba za kulelea wazee za kutosha kulingana na idadi ya wazee waliopo katika mkoa husika ili kuwasaidia wazee ambao wanahitaji kulelewa.

Mheshimiwa Spika, nimalize kwa kuchangia suala la ukatili kwa wanawake na watoto. Kumekuwa na wimbi kubwa la wanaume kupiga wake zao na watoto hata kupelekea kupata ulemavu, niiombe Serikali itunge sheria kali ili kudhibiti ukatili huu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Rais wetu Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anazozifanya katika Taifa hili Mungu aendelee kumlinda na kumbariki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Makamu wa Rais, nimpongeze Waziri Mkuu, Baraza la Mawaziri, Spika na wewe Naibu Spika kwa kazi nzuri mnazozifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya pongezi hizi nianze kuchangia katika Sekta ya Maliasili na Utalii. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa jitihada zake za kuitangaza Tanzania kimataifa kupitia programu yake ya Royal Tour nakuiingizia nchi yetu mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mafanikio tunayoyapata, tunapata lakini pia tuna changamoto za wanyamapori. Kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa wananchi wanaoishi kwenye mipaka ya hifadhi. Kumekuwa na matukio makubwa mawili ya Tembo kuua wananchi na Tembo kuharibu mazao ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Kilimanjaro tunazo wilaya tatu ambazo ni Wilaya ya Rombo, Mwanga na Same ambazo zinaathirika sana na wanyamapori. Katika Wilaya ya Same vijiji vya Mahore, Muheza, Kihurio, Bagamoyo, Kalamba na Kadando vimekuwa vikiathirika sana na wanyamapori hawa kwa kusababisha vifo kwa wananchi pamoja na uharibifu wa mazao yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatoa fidia, fidia inayotolewa na Serikali ni Sh.25,000 endapo mwananchi atakuwa ameharibiwa zao lake kwa hekari moja. Hivi tunavyoongea nimepata malalamiko kutoka kwenye Kijiji cha Mahore, aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mahore ametuma meseji kwamba tuombe msaada kwa kuwa askari wa wanyamapori wamezidiwa na tembo na hivyo wananchi wa maeneo hayo wameacha kazi zao na kwenda kulinda tembo ili kuhakikisha kwamba mazao yao yanakuwa. Naomba sana Serikali iangalie suala hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo Serikali inatoa Shilingi Milioni Moja kama kifuta machozi kwa mwananchi ambaye ameuawa na tembo. Kulingana na hali ya maisha ambayo tunayo sasa hivi na kupanda kwa vitu, viwango hivi tukiviiangalia haviendani na hali ya maisha. Baba huyu au Mama huyu ambaye atuuawa na tembo, ameacha familia ambayo yeye ndiye alikuwa akitegemewa kiasi cha Shilingi Milioni Moja hakiwezi kusaidia chochote. Naiomba Serikali yangu sikivu, iangalie kwa makini fidia hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote Serikali hii sasa hivi tunayokwenda nayo ya Mama Samia Suluhu Hassan, ni lazima tumpongeze kwa kuwa anajaribu sana kutatua matatizo ya Hifadhi za Wanyama. Tushirikiane Serikali pamoja na wananchi ili tuangalie ni nini ambacho kinaweza kuzuia wale wanyama wasisogee katika makazi ya wananchi ili kulinda mali zao pamoja na uhai wao. Niiombe Serikali kupitia Bunge hili Bajeti ya 2022/2023 iongezwe katika sekta hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya mchango huo naomba sasa niende katika sekta ya barabara. Niendelee kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kazi nzuri ambayo imefanya, kwa kujenga barabara zetu nchini kote. Niiombe Serikali imalize barabara ambazo zimejengwa vipande vipande ili ziweze kumalizika na wananchi waweze kufaidi katika shughuli zao za ujenzi wa Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee barabara ambayo imejengwa vipande vipande barabara ya Same – Mkomazi. Hivi karibuni Kamati yangu ya Uwekezaji Mitaji ya Umma tukiwa kwenye ziara tulitembelea Hifadhi ya Mkomazi. Katika mojawapo ya mambo ambayo wameomba Serikali iwasaidie ni barabara ya Mkomazi - Same. Wamedai barabara ile ni fupi kwa wale ambao wanatokea Tanga na Dar es Salaam wanaifahamu, lakini wamesema watalii wengi wanaotokea Dar es Salaam na Tanga wanapenda barabara ile kwa kuwa ni fupi, lakini barabara ile imejengwa vipande kwa vipande, imeanza Kiurio kipande, ikaachwa Ndungu kipande, Maore kipande, Kisiwani kipande.

Mheshimiwa NaibU Spika, hivyo wanaiomba Serikali Hifadhi ya Mkomazi Game Reserve imetuma Kamati ya PIC, Mwenyekiti wangu yupo pale atathibitisha kauli hiyo. Tuiombe Serikali ili watalii wale waweze kupita njia iliyo rahisi kufika katika hifadhi na barabara ile ikiboreshwa kwa madai yao watalii wetu watapata urahisi wa kufika katika hifadhi vizuri na kwa usalama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niendelee kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana inazofanya na niendelee kuiomba Serikali iangalie yale matatizo ambayo yanawagusa sana wananchi wa Tanzania, kama vifo na kuharibiwa mali zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie taarifa ya mwaka 2020/2022. Kwanza napongeza Kamati zote tatu kwa mawasilisho yake mazuri. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PIC, nitachangia yale ambayo tumeyaongelea katika Kamati yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitachangia katika maeneo matatu. La kwanza ni changamoto ya mitaji katika taasisi; ya pili, ni TANAPA na ya tatu ni mali ghafi katika viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, naanza na changamoto za mitaji. Tunalo Shirika la TEMESA. Shirika hili linafanya kazi ya kutengeneza magai ya Serikali yaliyo mengi pamoja na kampuni. Serikali imewekeza mtaji na linajiendesha mpaka sasa hivi shirika hili linasuasua, limekuwa na madeni makubwa ambapo Serikali hii ambayo imewekeza, imeikopa taasisi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka dakika hii TEMESA inadai shilingi milioni 45.39. Haiingii akilini kwamba sasa hivi kule ambako tunategemea tupeleke magari yetu TEMESA wao wanafika mahali hata vipuri vya kutengenezea magari yetu hawana. Wanashindwa hata kutoa gawio katika Mfuko wa Serikali kuu kwa kuwa hawana fedha za kuendeshea taasisi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya uchambuzi wa Kamati tunaishauri Serikali ihakikishe kwamba inalipa madeni yote ya TEMESA na kuhakikisha kwamba inatengeneza utaratibu mzuri ambao utakuwa ni utaratibu wa prepaid yaani tengeneza, lipa, ili kuhakikisha kwamba madeni mengine hayazalishwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuchangia TEMESA, nakuja katika Shirika la Hifadhi, TANAPA. Wabunge wengi wamesimama kuongolea suala la TANAPA. Mwanzo TANAPA ilikuwa ina hifadhi 16, mpaka sasa hivi ina hifadhi 22, lakini kwa bajeti ile ile ambayo ilikuwa inaendeshea ikiwa na hifadhi 16.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba kwa sasa ongezeko la hifadhi sita halitatosheleza bajeti ya kuendeshea shirika hilo. Ikumbukwe kwamba kuna changamoto mbalimbali ambazo barabara zetu zinazoingia katika hifadhi siyo rafiki, hivyo zinahitaji kufanyiwa ukarabati ili kuleta tija hasa watalii wetu wanapokuja kutembelea wanyama.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna changamoto nyingine ambayo ni maji. Serikali inabidi ijipange katika kujenga mabwawa ili kuepusha ule utamaduni ambao naweza nikauita utamaduni wa wanyama kutoka katika hifadhi na kuja katika makazi ya watu na baadaye kuleta athari ya watu kufariki na kuharibiwa mali zao. Kamati imechambua kwa kina, inaishauri Serikali ihakikishe kwamba inaongeza fedha za kutosha katika shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika viwanda vyenye changamoto ya mitaji. Nichangie kuhusu Kiwanda cha Ngozi cha Kimataifa cha Kilimanjaro kilichopo Manispaa ya Moshi Kata ya Karanga. Tulienda kutembelea kiwanda hicho, tulifika tukaona jinsi walivyo na vitu vizuri, na bahati nzuri pia walishakuja kutembelea Bunge wakaleta bidhaa zao tukaziona. Cha kusikitisha ni kwamba kiwanda hicho hakina malighafi za kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ukweli usiopingika kwamba Halmashauri zetu, Watanzania tunachinja sana ng’ombe na mbuzi. Ni vizuri Serikali ikajipanga sasa kupitia Halmashauri zetu, sekta ya mifugo wakahakikisha kwamba ngozi zile ambazo zinachinjwa zinahifadhiwa vizuri ili hatimaye ziweze kuja kuuzwa katika viwanda vyetu ili viweze kufanya kazi na vilete tija. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nami kunipatia nafasi nichangie hotuba hii ya Bajeti ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, Mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya katika Taifa hili na kutuletea fedha nyingi sana kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee Mkoa waa Kilimanjaro. Mkoa wa Kilimanjaro tumepata Shilingi bilioni 620.224 katika miradi 717. Tunampongeza sana Mama, tunaipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Naomba nifafanue miradi hii. Afya tumepata shilingi bilioni 45, elimu tumepata shilingi bilioni 17.21, ujenzi tumepata shilingi bilioni 126, nishati tumepata shilingi bilioni 21.59, maji tumepata shilingi bilioni 358.43, uchumi tumepata shilingi bilioni 17.63, ardhi tumepata shilingi bilioni 11.3, utawala tumepata shilingi bilioni 3.97. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa fedha hizi ambazo tumezipata kwa kuwa haijawahi kutokea, ni jambo la kihistoria. Baada ya pongezi hizi na fedha hizi ambazo tumezipata, nitajikita katika sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya kazi kubwa sana katika sekta ya afya, tumejenga zahanati, tumejenga vituo vya afya, tumejenga hospitali za wilaya, za mikoa na za rufaa. Hata hivyo, bado tuna changamoto ambazo hospitali hizi zinaikabili. Kwanza kabisa tuna changamoto ya watumishi, hasa katika ngazi za kata katika zahanati. Ni ukweli usiopingika kwamba tunao watumishi wachache sana hasa katika sehemu za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna changamoto ya nyumba za watumishi. Unakuta daktari amehamishiwa zahanati fulani, lakini anatumia kilometa kama moja na nusu kutembea kila siku kufika katika kituo chake cha kazi. Naiomba Serikali iliangalie hili kwa kina kirefu, kwa mapana yake ili madaktari hawa waweze kufanya kazi vizuri na kuwahudumia wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende katika Hospitali ya Rufaa ya Mawenzi. Nilisimama tena hapa kuongelea kuhusu Hospitali hii ya Mawenzi ambayo ni Hospitali ya Mkoa. Nashukuru Serikali kwa kuwa imefanya kazi kubwa sana katika jengo la mama na mtoto, linaendelea vizuri na kazi inaendelea. Pia, naishukuru Serikali kwa Shilingi bilioni 1.5 ambayo wametupatia kwa ajili ya ujenzi wa wodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Hospitali hii ya Mawenzi ni hospitali ambayo imejengwa kipindi cha mkoloni, majengo yake yamechoka sana na hayana hadhi ya kuitwa Hospitali ya Mkoa. Naiomba Serikali ijitahidi kuendelea kutoa fedha kwa ajili ya wodi zilizoko pale ili angalau ziweze kujengwa zifanane na hadhi ya Hospitali ya Mkoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee changamoto iliyopo katika Hospitali ya Mawenzi ambayo ni jengo la kuhifadhia maiti (Mortuary). Kama nilivyotangulia kusema kwamba majengo mengi yalijengwa kipindi cha mkoloni. Jengo hili kwanza ni dogo, lakini pia ni la zamani, hata majokofu yaliopo pale yamechoka. Hospitali ile ya Mawenzi ni ya Mkoa. Tunazo wilaya saba katika Mkoa wa Kilimanjaro, wote wanaitegemea ile hospitali, lakini yanapotokea matatizo ya watu kufariki, nasikitika sana kwa sababu hata hospitali ile inazidiwa kiasi kwamba miili ile ya marehemu itafutiwe nafasi kupelekwa kwenye Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya KCMC, jambo ambalo unakuta sasa nyingine hata kule KCMC kumejaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi, naamini ni Serikali Sikivu, iangalie Mkoa wa Kilimajaro na ile Hospitali ya Mawenzi ili iweze kutusaidia sehemu hii ya mortuary. Kwanza tujengewe mortuary kubwa ambayo itakuwa na hadhi ya mkoa na itakayokuwa na majokofu mengi na imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia baada ya kuchangia kuhusu Hospitali ya Mawenzi kwa maana ya afya, naomba nije katika ukatili dhidi ya watoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mwanamke na ninaposema suala la mtoto, niseme wote ni wazazi, Wabunge wenzangu wanaume msije mkasema lakini wanaume sisi; wanawake inatugusa zaidi. Inatugusa kwa ile amini tuliyokula ya kukaa na watoto tumboni miezi tisa na kuwalea mpaka watakapofika hatua ambayo wanajitambua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ukatili wa watoto kwa kweli limekithiri sana hapa nchini. Mimi kama Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kilimanjaro, nilifanya ziara katika Mkoa mzima wa Kilimanjaro nikiambatana na watumishi wa Dawati la Kijinsia katika Wilaya zote. Nasikitika mambo ambayo tulikuwa hatutegemei kwamba yanaweza kufanyika yanafanyika katika Mkoa wa Kilimanjaro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba kama Wabunge wote hatutakuwa na sauti moja, tukashikana, suala hili hatutaweza kulimaliza. Ninasema hivyo kwa sababu gani? Kumekuwa na utamaduni katika baadhi ya maeneo; niiseme Kilimanjaro. Baadhi ya watumishi wamekutana na changamoto ambayo mimi binafsi imeniwia ngumu. Nasema hivyo kwa sababu wanasema, baada ya kukutana na hoja kama hizo watoto wamefanyiwa ukatili, wanapokwenda kufuatilia, unakuta kwamba wale wazazi wanakutana wenyewe, wanayaongea wenyewe na zile kesi kule mahakamani hatimaye zinafutwa. Naiomba Serikali, kesi kama hizi zikipelekwa pale zifanyiwe uharaka ili ziishe haraka ili watu wasipotoshe Ushahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani kidogo, mimi ni Mpare nimeolewa na Mchaga, ni waume zangu, lakini wana utamaduni ambao mimi binafsi siupendi. Kule Uchagani unapofanya jambo ambalo linakuuma sana au ni zito, kuna jani moja linaitwa sale. Ukiiongea na watumishi wale, dawati la jinsia watakwambia tatizo hilo. Wanapokuta mambo yamekuwa siyo mazuri, linatumika jani la sale kwenda kuomba msamaha ili mambo yaishe. Wakati huo tayari watoto wameshaathirika. Nawaomba ndugu zangu tusitumie vitu vya mila kuharibu vizazi vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisemea hili kwa sababu haiingii akilini uletewe sare wakati mtoto wako amelawitiwa, ni jambo la kusikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee pia…

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii ya kilimo. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia kufika siku hii ya leo, lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa jinsi alivyoiongeza bajeti ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwashukuru na niwapongeze Mawaziri, Mheshimiwa Bashe, Mheshimiwa Mavunde pamoja na watendaji wote ambao wanaifanya kazi ambayo Watanzania wote wanaiona, kazi inayofanyika katika Wizara hii ya Kilimo. Mimi nitachangia kuhusu zao la parachichi Mkoani Kilimanjaro, nitachangia kuhusu umwagiliaji wa zao la mpunga na nitachangia kuhusu Benki ya Wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na zao la parachichi Mkoani Kilimanjaro. Sisi Wanakilimanjaro tunaona wivu wa kilimo wa zao la parachichi. Zao la parachichi aina ya Has ni zao ambalo sasa hivi linawika sana, linauzwa nje ya nchi, linaingiza kipato kwa mkulima mmoja mmoja na Taifa kwa ujumla, lakini zao hili kule kwetu bado kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, viko vikundi ambavyo vinazalisha mbegu ya has, lakini vikundi hivi pamoja na kuzalisha mbegu hiyo, bado bei yake ni kubwa sana, bei ya mche mmoja inaanza kuanzia Sh.6,000/=, Sh.5,000/=, ukiomba sana Sh.4,000/=. Kwa mwananchi wa kawaida wa hali ya chini kutoa Sh.6,000/= au Sh.5,000/= au 4,000/= kununua mche mmoja kwa kweli ni mtihani mkubwa. Tuiombe Serikali sasa itoe ruzuku kwa vile vikundi ambavyo vinazalisha miche ili viweze kuzalisha kwa wingi, ili pia viweze kuuzia wananchi kwa bei nzuri ambayo zao hili litalimwa kwa wingi sana na litawaingizia kipato na kukuza uchumi kwa mtu mmojammoja na Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongelea kuhusu zao la parachichi, nitaongelea kuhusu zao la mpunga. Katika Mkoa wa Kilimanjaro tuna mabonde mengi sana, tuna mabonde ambayo yanafaa kilimo cha mpunga na tuna mabonde ambayo pia hayo hayo yanafaa kilimo cha vitunguu, lakini hatuna skimu za umwagiliaji za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kilimanjaro ni wakulima wazuri sana wa wa mpunga na kama tunavyotambua kwamba, kilimo cha mpunga ni kilimo ambacho ni cha chakula pamoja na biashara. Kwa maana hiyo, basi, tunaiomba Serikali kule ambapo tunayo mabonde mengi ambayo hayana skimu, Serikali isaidie kujenga skimu za umwagiliaji, ili kukuza kilimo cha mpunga katika Mkoa wa Kilimanjaro. Hii itasaidia wananchi mmoja mmoja kuongeza kipato na Taifa kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nakuja kwenye suala la Benki ya Kilimo. Ni ukweli usiopingika kwamba, unaposema kilimo ni vijijini, lakini benki hizi ziko maeneo ya mjini. Wakulima wengi wanatamani sana kukopa, lakini je, wanafikaje mjini? Kuna mkulima ambaye anakaa kule Gonja Maore hajui Makao Makuu ya Mkoa, Moshi. Kuna mkulima anakaa kule Mamba Juu hajui Makao Makuu ya Wilaya, Same. Huyu mkulima ambaye ndiye mkulima anayetarajiwa alime ili auze, je, anaifikiaje hii benki? Naiomba Serikali hii sikivu, iangalie sana suala hili la kuwapelekea huduma kwa karibu walengwa wa kilimo kwa maana ya wakulima katika maeneo yao, ili waweze kulima na kuuza mazao yao katika masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, niongelee suala la masoko. Ni ukweli kwamba, wakulima wanajitahidi sana kulima, lakini hapo katikati kuna masuala ambayo yanajitokeza katika kutafuta masoko. Wanaofaidi nguvu za wakulima ni madalali. Mkulima atachukua muda mrefu wa kulima mpaka kuvuna, lakini dalali atakuja atanunua gunia la mpunga au la tangawizi au la mahindi kwa bei ndogo sana na akienda kuuza zao hilo atapata faida zaidi ya mara mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali iangalie sana. Kama ambavyo tumeongeza bajeti ya kilimo, lakini pia tuangalie suala la masoko ili tuweze kumkomboa mwananchi au mkulima huyu katika suala zima la kuuza mazao yake. Pia tuangalie suala la lumbesa, lumbesa kila mtu anaisema. Wafanyabiashara wanafaidika, wakulima wanaumia. Ifike mahali sasa Serikali itoe tamko kwamba, mizani ipelekwe katika maeneo ya kuuza na kilo ya gunia moja, kama inavyofahamika, kilo 100, ndio kilo halali ya zao la aina yoyote. Masuala ya lumbesa tuhakikishe kwamba, sisi tunayakomesha ili kuwasaidia wakulima wadogo wadogo kuuza mazao yao kwa bei nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongea hayo, naomba pia niipongeze Serikali kwa jinsi ambavyo imeweza kupeleka miradi katika Mkoa wa Kilimanjaro. Serikali imepeleka miradi katika wilaya mbalimbali katika Mkoa wa Kilimanjaro ikiwepo Same, Mamba Miamba, ikiwepo Kalemawe, Wilaya ya Same, Manispaa ya, I mean Moshi DC…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Zuena, muda wako umeisha, unga mkono hoja.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naunga mkono hoja naipongeza Serikali kwa kazi nzuri inayofanya katika Wizara ya Kilimo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na mimi kunipa nafasi ya kuchangia Bajeti ya Wizara ya Habari Mawasiliano na Teknolojia ya Habari. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika kuifungua Tanzania kwa njia ya mawasiliano. Nimpongeze Waziri Mkuu, nimpongeze Waziri Nape, nimpongeze Waziri Kundo pamoja na watendaji wote wa sekta hii ya Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo nitachangia kuhusu usikivu wa redio ya TBC katika maeneo ya mipakani, ukosefu wa mawasiliano katika maeneo ya mipakani pamoja na Hifadhi ya Mkomazi ambayo jina lake maarufu kwa kule kwetu inaitwa Kambi ya Simba.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kuhusu ukosefu wa mawasiliano ya redio ya Taifa (TBC). Katika Mkoa wa Kilimanjaro maeneo ya mipakani hatuna usikivu kabisa wa redio yetu, mara nyingi ukifungua redio unasikiliza redio za kenya kitu ambacho Watanzania wanakosa kupata Habari ya nchi yao. Jambo hili tumekuwa tukiliongea, mimi binafsi nimeliongelea sana hapa katika Bunge hili lakini hata leo hii katika Mkoa wa Kilimanjaro maeneo ya Rombo, Vijiji vya Kikererwa na vijiji vingine jirani ambavyo viko mpakani hawasikii kabisa redio yetu ya TBC.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali, katika minara hii ifanye jitihada ya kupeleka minara hiyo katika maeneo hayo ili na sisi Watanzania tujivunie shirika letu la mawasiliano jinsi linavyofanya kazi kuliko tukikaa kule tunasikiliza redio za wenzetu hatupati habari zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi tena katika mawasiliano maeneo hayohayo. Safaricom imekuwa ikitawala sana maeneo haya, kiasi kwamba hata mtu akiwa yuko kule kijijini hawezi kupata mawasiliano ya Vodacom, Tigo na kampuni nyingine za Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme walinzi wakubwa wa mipakani ni wananchi wanaoishi kule. Kwa hiyo kwa kukosa mawasiloiano kwao tunakosa hata kupata taarifa mapema pale ambapo panakuwa na changamoto yoyote katika maeneo ya mipakani. Niiombe Serikali katika minara hii 758 wahakikishe sasa kwamba maeneo yote ya mipakani yanapata minara ili Watanzania na sisi tuweze kupata huduma stahiki ya mawasiliano katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika maeneo ya Hifadhi ya Mkomazi. Nimesimama hapa Bungeni zaidi ya mara mbili nikiongelea changamoto ya mawasiliano katika Hifadhi ya Mkomazi. Hifadhi ile inawanyama wakali, hifadhi imetokea kuwa na changamoto nyingi za wananchi kuporwa mali zao, hifadhi ile hata Askari wa Wanyamapori maeneo yale walituomba sisi kama Kamati tusaidie ili waweze kupata mawasiliano kwa kuwa inaweza ikatokea changamoto yoyote ndani ya hifadhi lakini hawana mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali yangu sikivu Serikali ya Chama Cha Mapinduzi; Mheshimiwa Rais ameshuhudia utiaji saini wa minara 758. Katika minara hiyo niiombe sana Serikali iangalie maeneo ya hifadhi kwa kuwa kule ndani ya hifadhi kunakuwa na changamoto nyingi. Inaweza ikatokea hata Wanyama wakali lakini utoaji wa taarifa ukawa ni hafifu sana hivyo niombe katika minara hiyo 758 serikali itupe jicho katika Hifadhi ya Mkomazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nichangie kuhusu suala la wizi wa mitandaoni. Ni ukweli kwamba vijana wengi wanatumia kuibia wananchi katika mitandao unaweza ukafungua simu ukaambiwa nitumie pesa kwa namba hii hii jina litatoka fulani fulani fulani. Mheshimiwa Nape nakuamini Waziri wangu, Mheshimiwa Kundo nakuamini Waziri wangu, ninyi ni vijana mmepewa hii Wizara kwa kuwa ni vijana ambao ni wachapakazi hakikisheni kwamba kazi hii wanayoifanya matapeli wanataka kuwazidi akili. Msikubali kabisa hali hii ya wizi wa kutumia simu nchini Tanzania ukaendelea, udhibitini. Naamini mnao uwezo wa kufanya hivyo ili wananchi waweze kuishi vizuri na kuona kwamba wizi huu umetokomea.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo na mimi naungamkono hoja, lakini nitaomba Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapa uwaeleze Watanzania hasa wa Mkoa wa Kilimanjaro…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: …ni lini wataondokana na adha ya kusikiliza safari com badala ya Vodacom na mitandao mingine ya Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia bajeti hii ya Seikali. Nianze kuipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na Mama yetu Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri sana anazozifanya. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kutuletea bajeti hii, bajeti ambayo imekonga mioyo ya Watanzania wote. Pia nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na Watendaji wake wote wa Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa mikopo ya halmashauri; mikopo hii ya halmashauri imekuwa ikiwajenga sana akina mama kiuchumi. Akina mama wengi wamechukua mikopo hii na wanalea familia zao na wanasomesha watoto Tanzania nzima.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wanawake ambao tupo hapa Bungeni ni wawakilishi wanawake wenzetu, tumekuja ili tuwasaidie na wenyewe waweze kunyanyuka kiuchumi. Mikopo hii ya 4:4:2 wanawake asilimia nne, vijana asilimia nne na wenye ulemavu asilimia mbili bado imekuwa haitoshi, kwa sababu wanawake wengi wanaopata hii mikopo wanafanya biashara na wanapofanya biashara wakirudisha ile mikopo unakuta vikundi vingi vimejiunga na bado fedha haitoshelezi. Niiombe Serikali iache mikopo hii utaratibu huu wa 4:4:2 na wamachinga Serikali kuu iwatafutie fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kutoka katika mchango wangu wa kwanza nije katika sekta ya uvuvi; nitaomba kuchangia Ziwa Jipe. Ziwa Jipe lipo katika Mkoa wa Kilimanjaro katika Wilaya ya Mwanga. Naongea kwa masikitiko makubwa sana, na Wabunge wenzangu nawaomba mtusaidie katika ziwa hili. Ziwa Jipe lipo katikati ya mpaka wa Kenya na Tanzania, lakini Ziwa Jipe limekuwa na magugu kiasi kwamba shughuli zote za uvuvi pale hakuna tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, ikumbukwe kwamba chanzo cha maji cha Ziwa Jipe kinatoka katika Mkoa wa Kilimanjaro, lakini wenzetu upande wa pili wametengeneza mazingira mazuri, wametengeneza miundombinu ya utalii wana hoteli za utalii, wanafaidika kupitia chanzo chetu cha maji ambacho kinatoka Mkoa wa Kilimanjaro. Lakini kwetu sisi magugu maji yamezidi kiasi kwamba hata wakazi wa pale hata kuvua samaki wameshindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, walishafika viongozi wa mazingira akiwemo Mheshimiwa Waziri Makamba na Mheshimiwa Waziri Chande, wamefanya vikao na Vijiji vya Butu ambavyo vimezunguka Ziwa lile la Jipe. Lakini wamewapa wananchi matumaini, kwa sababu wananchi wanapoona viongozi wa juu wakija wanapata matumaini kwamba angalau tumesikilizwa shida yetu itatekelezwa. Hivi ninavyoongea wale Wapare hata Samaki kwa ajili ya chakula hawawezi kuvua

Mheshimiwa Naibu Spika, niiombe Serikali iangalie kwa kina sana na ifanye haraka iwezekanavyo kutoa yale magugu kwa kuwa Ziwa lile la Jipe ndilo linaloshisha Bwawa la Nyumba ya Mungu. Bwawa la Nyumba ya Mungu linazalisha umeme megawatt tano mpaka nane; lakini bwawa lile sasa hivi pia kutokana na yale magugu ambayo maji yanashindwa kupita vizuri maji yake yanaenda yakipungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni hivi karibu tu Mheshimiwa Rais alipitisha kwamba, mradi wa maji unaokwenda kuanzia Same, Mwanga, Korogwe umetengewa fedha. Sasa fedha hizo zimetengwa, mradi huo wa maji unategemea maji hayo ambayo yanatoka katika Ziwa Jipe. Niiombe Serikali itusikilize sana kilio hiki na niombe Waziri atakapokuja ku-windup atueleze ni lini lile Ziwa Jipe litatolewa magugu, Wapare wamechoka, wanashida hata Samaki kwa ajili ya chakula hawapati.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja.