Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon Kassim Hassan Haji (6 total)

MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Kituo cha Polisi Mwanakwerekwe ambacho kiliwekwa jiwe la msingi mwaka 2008 na Kiongozi wa Mbio za Mwenge?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa wananchi wa Jimbo la Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Naibu Spika, Mwanakwerekwe kuna Kituo cha Polisi cha Daraja ā€œCā€ ambacho kinatumika hadi sasa na kinafanya kazi kwa saa ishirini na nne, na eneo hilo lilitolewa na Serikali baada ya kuhamisha Idara ya Maonyesho Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo la Magogoni Amani kwa Mabata ndiko kuna jengo la kituo kidogo cha polisi, ambacho kinajengwa kwa nguvu za wananchi na jiwe la msingi liliwekwa na Kiongozi wa Mbio za Mwenge mwaka 2008 na ujenzi wake umefikia kwenye hatua ya renta. Serikali kupitia Jeshi la Polisi inatafuta fedha ili kumalizia ujenzi wa kituo hicho kiweze kuhudumia wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuongeza maduka ya kutolea dawa kwa kutumia Bima ya Afya ili kuondoa usumbufu wanaopata wananchi wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA AFYA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Afya, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba idadi ya maduka na vituo vinavyotoa huduma za Bima ya Afya Zanzibar ni vichache ambapo kwa kipindi cha miezi sita kuanzia Juni, 2021 hadi Desemba 2021 idadi ya vituo vimeongezeka kutoka 19 hadi 65.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuhamasisha wamiliki wa vituo vya kutolea huduma za afya na maduka ya dawa kujiunga na huduma ya bima ili kuwafikia wananchi wote. Ahsante.(Makofi)
MHE. HASSAN HAJI KASSIM aliuliza: -

Je, kuna mkakati gani wa kuitanua sehemu ya kusafirishia abiria wanaokwenda Zanzibar katika Bandari ya Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Haji Kassim, Mbunge wa Mwanakwerekwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali kupitia TPA imetenga kiasi cha Sh.1,500,000,000 kwa ajili ya maboresho ya sehemu ya abiria katika Bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, hatua iliyofikiwa sasa ni manunuzi ya Mkandarasi kwa ajili ya maboresho ya eneo la kusafirisha abiria kwenda Zanzibar. Maboresho yatahusisha ukarabati wa miundombinu ya gati la kuhudumia abiria ikiwa ni pamoja na ujenzi wa jengo jipya la abiria ili kuongeza uwezo wa kuhudumia abiria, kuweka mkanda wa mizigo (conveyor belt), ukarabati wa kingo za gati, maboresho ya sehemu ya abiria mashuhuri (VIP), sakafu na vyoo. Aidha, Mkandarasi anatarajiwa kupatikana na kuanza kazi mwezi wa Desemba, 2022.
MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA K.n.y. MHE. HASSAN HAJI KASSIM aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka utaratibu wa kuwa na kitambulisho kimoja chenye taarifa zote za huduma ndani ya kadi moja?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Haji Kassim, Mbunge wa Jimbo la Mwanakwerekwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA) inatengeneza vitambulisho vya Taifa kwa kutumia teknolojia ya smart card ambapo kitambulisho kinakuwa na chip inayokiwezesha kutumika kwa matumizi mbalimbali. Kitambulisho hiki kinaweza kutumika kama pochi ya fedha ya kielektroniki (E-Wallet), Atm card kwa ajili ya kutoa fedha kutoka mashine ya ATM, huduma za Bima ya Afya, Kitambulisho cha Mpiga Kura na mengineyo.

Mheshimiwa Spika, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupitia NIDA inaendelea kufanya mawasiliano na taasisi nyingine zenye vitambulisho ili kuona uwezekano wa kuoainisha taarifa zilizomo katika vitambulisho tofauti kwa madhumuni ya kuwa na kitambulisho kimoja. Mara muafaka utakapofikia wananchi watajulishwa rasmi lini utaratibu huo utaanza kutekelezwa. Ninashukuru.
MHE. RASHID A. SHANGAZI K.n.y. MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kubadili utaratibu wa malipo kwa wastaafu wa Jeshi la Polisi wa Zanzibar ili kuondoa usumbufu wanaoupata?
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali utumishi wa Askari Polisi ulikuwa kwenye masharti ya pensheni na bakshishi. Askari ambaye hakuwepo kwenye masharti ya pensheni alifanya kazi kwa mkataba wa miaka 12 kwa kujaza mkataba wa kipindi cha kila baada ya miaka mitatu kumalizika. Kwa mujibu wa Sheria ya Jeshi la Polisi na Polisi Wasaidizi Sura ya 322, askari kwa hiari yake mwenyewe baada ya mkataba alipaswa kufanya chaguo la ama kuendelea na utaratibu wa ajira ya mkataba na kwa malipo ya bakshishi ambao ukomo wake wa utumishi ni miaka 21 au kuingia kwenye utaratibu wa ajira ya malipo ya pensheni na kulipwa mafao ya uzeeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni Jeshi la Polisi limefanya maboresho kwa kuondoa utaratibu wa mkataba wa miaka 12 na kuwa miaka sita pamoja na kuondoa chaguo. Na baada ya mkataba kumalizika askari wote wanaingia kwenye ajira ya kudumu yaani pensheni.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, lini Serikali itafanya maboresho ya Sheria ya Mfuko wa Jimbo ili kuondoa kikwazo cha utekelezaji Zanzibar kwa kuwa Wabunge siyo Madiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais ā€“ TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Haji Kassim, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko wa Jimbo Na. 16 ya mwaka 2009, uidhinishwaji wa vipaumbele na matumizi ya fedha hufanywa na Kamati ya Mfuko wa Jimbo yenye wajumbe saba, akiwemo Mbunge wa Jimbo husika ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati. Aidha, Kamati ina jukumu la kupokea, kujadili vipaumbele vya miradi iliyowasilishwa na wananchi na kuidhinisha miradi itakayotekelezwa.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya jimbo inatekelezwa sambamba na Sheria ya Fedha, Sheria ya Manunuzi ya Umma pamoja na Miongozo mbalimbali ya Mipango, Bajeti na Matumizi ya fedha za Umma. Hivyo, utaratibu uliopo kisheria unamwezesha Mbunge wa Jimbo husika kutimiza wajibu wake wa kupokea maombi, kuweka vipaumbele na kuidhinisha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa vipaumbele vilivyokubaliwa, ahsante.