Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Ally Juma Makoa (19 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kuniona. Awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema zake mbalimbali anazotujaalia, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kumuumba mja wake Dkt. John Joseph Pombe Magufuli na akamjaalia kuwa Rais wa nchi hii na yeye akaitendea haki nchi hii kwa kufanya mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ndiyo mara yangu ya kwanza pia kusimama katika Bunge lako hili,nikishukuru chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa kuniteua na kunifanya kuwa Mbunge. Pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kondoa Mjini kwa kuniamini na kunipa kura nyingi za kishindo na mimi kuwa mwakilishi wao.Ahadi yangu kwao ni kwamba tutafanyakazi kwa bidii kubwa kuhakikisha tunaleta maendeleo kwa wananchi. Vile vile niishukuru familia yangu mama Hashim na watoto wangu wawili kwa kuendelea kunipa nguvu katika kufanyakazi za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimepitia hotuba zote mbili za Mheshimiwa Rais ile ya 2015 na hii kwa kweli hotuba zote mbili hizi zimejaa kila aina ya miongozo kwa ajili ya kuliletea neema Taifa hili. Ukweli ni kwamba pamoja na michango yetu yote tutakayochangia bado haitoi maana ya kwamba Serikali hii ya Awamu ya Tano, imefanya mambo makubwa sana katika Taifa hili. Hivyo basi, katika kuchangia mimi nitakwenda ukurasa wa 10, Wizara ya Afya. Serikali ya Awamu ya Tano imepunguza kwa kiwango kikubwa sana vifo vya mama wajawazito na watoto wa umri wa chini ya miaka mitano. Kama tutamsaidia Mheshimiwa Rais kikamilifu basi tutaendelea kupunguza vifo hivi, lakini kama tutazembea, hatutaweza kumsaidia Mheshimiwa Rais, bado vifo hivi vitaendelea kupanda.

Mheshimiwa Spika, kwenye hiki kifungu cha akinamama wajawazito kumekuwa na malalamiko makubwa sana kwa wananchi kwamba sera za afya na Ilani ya CCM, utekelezaji wa sera unakinzana na Ilani ya CCM, Ilani ya CCM inaelezea kwamba tutaendelea kutoa huduma bure kwa akinamama wajawazito na watoto wa umri wa chini ya miaka mitano,lakini uhalisia haupo hivyo. Akinamama wamekuwa wakitozwa gharama katika kujifungua na akinamama wengi katika ziara zangu wamekuwa wakizungumza wengine wameamua kusimamisha kujifungua kwasababu ya gharama kubwa za afya.

Mheshimiwa Spika, juhudi za Serikali za kupunguza vifo zinaweza zikawa zinamikwamo kwasababu wapo akinamama ambao wameamua kujifungulia majumbani kwasababu wanaogopa kwenda kujifungua hospitali wakiogopa gharama. Sasa kama hili litaendelea na wakahamasishana akinamama basi juhudi za Serikali za kupunguza vifo hivi zitakuwa zimekwama.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Kondoa Mjini linaeneo ambalo limetengwa naMto Bubu. Miezi miwili iliyopita tumepata kesi za vifo, mama mjamzito akisubiria maji yapungue aende hospitali kujifungua maji hayakupungua akajifungulia upande wa pili wa barabara, mtoto akafariki,mama wakawa wanamkimbiza wampeleke Hanang, yule mama pia akafariki.

Kwa hiyo kutokana na hali hii iko haja ya Serikali kuona namna gani wanaweza wakasaidia ng’ambo ile ya Kata ya Serya ambayo haina kituo cha afya wala zahanati na wakati huo huo hawana uwezo wa kipindi cha masika kuja mjini kwaajili ya kutafuta huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, imekuwa ni kero kubwa sana katika maeneo hayo ambayo yanazungukwa na huo Mto Bubu. Kwahiyo ombi letu watu wa Kondoa tunaomba aidha yafanyike mambo mawili katika moja; kulijenga lile daraja ili watu waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi pamoja na kupata huduma za afya au kujenga kituo cha afya katika maeneo yale ya Serya.

Mheshimiwa Spika, eneo la kilimo wako wananchi ambao mashamba yao yaliharibiwa na tembo na wakaahidiwa muda mrefu sana watalipwa kifuta jasho. Mpaka leo watu wale wanadai, hawakulipwa fedha zao, lakini wananchi wa Kondoa wanalalamikia suala la kulipwa kifuta jasho.

SPIKA: Mheshimiwa Makoa, tembo walifika Kondoa Mjini?

MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, jimbo langu lina maeneo ya mjini na vijijini. Ipo Kata ya Kingale na Kata ya Serya ipo pembezoni mwa Hifadhi ya Swagaswaga. Kwa hiyo, tembo wale waliharibu mashamba ya watu lakini vifuta jasho wanavyopewa haviendani na thamani ya mashamba yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tunataka kupata mabilionea kupitia wakulima basi Wizara ione haja sasa ya kuangalia uwezekano wa kudhibiti tembo wale na kuwalipa wananchi fidia ya maeneo yao na siyo vifuta jasho. Kwa sababu kifuta jasho analipwa pesa ndogo sana ni bora alipwe fidia ili ile dhana ya kuwa na mabilionea kutokana na kilimo basi ipatikane.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni ajira kwa vijana. Serikali yetu imefanya vizuri sana kutenga asilimia 10 kwa ajili ya vijana. Hata hivyo, katika sera ya mfuko ule nashauri kwamba akaunti ya mikopo ya vijana ingetofautishwa na akaunti zingine za halmashauri ili wakati wa kupanga bajeti ya kuviwezesha vikundi asilimia 10 ya bajeti ya mwaka huu iwe inaendana na zile asilimia 10 zilizopita ambazo zimerejeshwa. Tofauti na ilivyo sasa asilimia 10 inayofanyiwa hesabu ya current year lakini yale marejesho yanaingia kwenye akaunti ya maendeleo. Kwa hiyo, tunashindwa kujua uhalisia hasa marejesho yamekuwa ni kiasi gani na asilimia kumi ya safari hii ni kiasi gani ili kuwawezesha wale vijana, kinamama na walemavu kuweza kupata fedha ambazo zitawasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, utaona vikundi vingi ambavyo vinapewa mikopo utakuta watu kumi wanapewa shilingi milioni 10, ukipiga hesabu ni shilingi milioni moja moja unashindwa hata kuwashauri wale vijana wafanye biashara gani. Mikopo hii maeneo mengi imekuwa siyo neema kwa vijana, wengi wamekimbia nyumba zao, wameshindwa kulipa madeni kwa sababu wanapewa mikopo kabla ya kupewa elimu ya kuifanyia kazi mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, niipongeze sana Serikali kwa namna ambavyo imefanya juhudi kubwa ya kujenga miundombinu ya barabara. Hata hivyo, kilio kilekile cha wananchi ni kwamba kipindi hasa hiki cha masika barabara nyingi hazipitiki. Kwa jimbo langu eneo ambalo linashughulikiwa na TANROADS mpaka sasa ni kilomita kama 0.8. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwa miaka yote mitano TANROADS wanaweza wasitie mkono au mguu katika jimbo langu. Eneo kubwa linachukuliwa na TARURA, uwezo wa TARURA ni mdogo kwa maana hiyo, tunaomba TARURA waongezewe nguvu kwa sababu barabara nyingi sasa hivi zinashikwa na TARURA.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Nami nianze kuchangia kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali yake yote kwa utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM na utekelezaji mzuri wa bajeti hii ambayo tunaendelea nayo. Pia nawapongeza Mawaziri na TAMISEMI wote kwa ujumla kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya kwa ajili ya utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata tukiwapongeza hapa, kutokana na muda wetu hatutakamilisha shukrani kwa sababu kwa kweli TAMISEMI katika bajeti hii wamefanya vizuri sana. Nimepitia utekelezaji kwa kuona kwa macho yale yote ambayo tuliyaomba, bajeti hii tunayoendelea nayo kwa kweli asilimia karibu 99 wameyatekeleza na miradi inaendelea kutekelezwa kwenye Jimbo langu kwenye Kata zote. Hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa katika bajeti hii inayoendelea, naomba mambo machache; moja, ni kwamba kuna shilingi milioni 130 zile kwa ajili ya ile Sekondari ambayo tunaendelea kuijenga. Pale kwenye Jimbo langu ile Sekondari ni kama imekamilika kwa sababu Naibu Waziri wa Elimu alipita juzi akaelekeza tuanze usajili. Kwa maana hiyo aliridhika na kiwango cha ujenzi wa ile Sekondari, na ninawakaribisha mje mwone namna watendaji wamepambana, ile Sekondari imekamilika na natarajia tuanze kuitumia mwezi wa Saba. Kwa hiyo, ile shilingi milioni 130 tunaomba ije kwa wakati ili tuweze kukamilisha katika kipande chetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upande wa bajeti hii tunayoendelea nayo, tunashukuru Serikali ilitupa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maabara mbili katika kila Sekondari, lakini tukumbuke kila Sekondari ina maabara tatu. Sasa tunamalizia majengo mawili na bahati nzuri huwa yanafuatana, linabaki moja. Kwa hiyo, tunaomba zile za ukamilishaji wa maabara ya tatu katika Sekondari na zenyewe zifanyiwe kazi mapema ili watoto wetu waweze kusoma kwa vitendo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika bejeti hii tunayoendelea nayo, tatizo la walimu ni kubwa, Waheshimiwa Wabunge wengi wamezungumza lakini sasa hapa nina ushauri kwamba, hebu wale walimu ambao wapo tayari mashuleni wanajitolea, wawe ni wa kwanza kuajiriwa kwa sababu unakuta wale walimu ambao wapo mashuleni na wamejitolea kufundisha wanakosa ajira lakini anapewa ajira mtu mwenye elimu, lakini kipindi hicho chetu usikute yuko kwenye maeneo tofauti ya kutafuta riziki, tunawaacha wale ambao wamejitolea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukianza na wale, maana yake hata shule zetu zitakuwa hazina upungufu wa walimu kwa sababu walimu wataona tukijitolea itakuwa ni kipaumbele katika kupewa ajira. Kwa hiyo, tujitahidi katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, masuala ya kwenye TARURA, nadhani tumefanya vizuri, lakini maeneo yetu ya mijini ambayo tunaratajia huo mradi wa TACTIC, ni vyema sasa nasi tukawahishwa. Tumepewa shilingi milioni 500, lakini maeneo mengine wamepewa shilingi bilioni moja kwa sababu tunatarajia tutapata huo mradi wa TACTIC kwa ajili ya barabara zetu za mijini; lami pamoja na taa na ujenzi wa stendi. Sasa tunatamani wananchi wajue, tunawaeleza kwamba tuna mradi huu utakuja, lakini sasa tufafanuliwe ni lini hasa tutaanza mradi huu katika Halmashauri zetu za Miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipitia bajeti hii ambayo sasa tunakwenda kuipitisha, nimeona yale ambayo mmetuwekea, tunashukuru na tunaona ni katika yale yale ambayo ni matarajio ya Wabunge pamoja na wananchi wanaowawakilisha. Hapa naomba Mheshimiwa Waziri alinukuu jambo hili liwe kama dharura kwake. Tuna Shule ya Msingi inaitwa Iboni. Nimeona hapa kuna fedha kwa ajili ya kukarabati shule zilizochakaa, lakini shule hii imechakaa over kuchakaa. Leo hata ukiwa na feni tu ukasema upulize kwa kasi kubwa, bati zote zile zinang’oka. Shule ile imejengwa miaka mingi sana; wamesoma babu zetu na baba zetu. Sasa hii siyo tu ku-repair, hii inahitaji madarasa ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu special zaidi, shule hii ina wanafunzi wa kawaida, lakini pia ina wenye mahitaji maalum na ndiyo shule pekee yenye watoto wenye uhitaji maalum. Pale wapo wasio na usikivu, wasioona, wenye mtindio wa ubongo. Bahati mbaya madarasa yao mawili yote yameanguka, leo wanasoma chini ya mikwaju, na hawa watoto ni maalum kabisa. Naomba jambo hili na lenyewe katika ile idadi ya madarasa, basi japo tupate madarasa yao mawili, ni muhimu sana kwa sababu watoto hawa ni wale wa uhitaji maalum. Kwa hiyo, natarajia Mheshimiwa Waziri atalichukua hili kwa msisitizo wake na tutawasaidia watoto wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda tena kuishauri Serikali kwamba sasa hivi tu-invest pia kwenye hosteli. Katika Halmashauri ya Mji, hatuna Sekondari hata moja yenye hosteli, lakini tunaona watoto wanashindwa kumaliza shule kutokana na mwendo wanaotembea. Wanaweza wakaanza shule watoto 60, wakamaliza 40, wengine wote wanaishia njiani. Kwa hiyo, nashauri, nami angalau pale Halmashauri ya Mji tupate japo hosteli, kuwe na sekondari japo moja yenye hosteli iliyokamilika, hasa hii sekondari mpya ambayo mmetuletea, ni shule ya kisasa sana, tukiijengea mabweni, kwa kweli itakuwa ni over shule; itakuwa ni shule zaidi ya shule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nigusie kidogo kwenye upande wa Madiwani. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI hawa Madiwani wanatakiwa wote wapewe heshima inayofanana. Bahati mbaya, sasa sijui ndiyo maelekezo ya TAMISEMI, kuna baadhi ya maeneo ya Halmashauri Madiwani hawa wanakuwa hawapewi thamani kama ile thamani ambayo Madiwani wa sehemu nyingine wanapewa. Mfano, unakuta Diwani anatoka kilometa 30, anakodi pikipiki shilingi 15,000/=; kwenda na kurudi ni shilingi 30,000/=; akifika kwenye Kikao anapewa posho ya shilingi 40,000/=. Kwa maana hiyo, Diwani huyu kweli anawezaje kwenda kutekeleza majukumu yake kwa kupewa posho ya shilingi 40,000/=? Ukiuliza, tunaambiwa ndiyo mwongozo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka tujue, ni kweli TAMISEMI mmewaongoza wao kuwalipa Madiwani posho shilingi 40,000 wakati Halmashauri nyingine wanalipwa kutokana na stahiki halali? Wengine wanalipwa posho shilingi 100,000/= na zaidi, lakini Halmashauri nyingine ikiwemo Halmashauri yangu, posho shilingi 40,000/= Diwani anatumia nauli kwenda na kurudi shilingi 30,000/=, itakuwa siyo sawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pengine utaona kwamba Wabunge wengi wamechangia kwamba Madiwani waongeze maslahi, ni kwa sababu mmepeleka fedha nyingi sana kule kwenye Kata ambazo zinasimamiwa na Madiwani, halafu Diwani unampa shilingi 40,000 au unampa shilingi 300,000 anakwenda kusimamia fedha nyingi, matokeo yake Madiwani wetu wanakata tamaa na wanakuwa hawafanyi kazi kwa ufanisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi sana nilitaka nielezee jambo moja. Kulikuwa na mchangiaji ambaye alizungumzia ujenzi wa stendi na soko la kisasa ambalo limejengwa Dodoma hapa; na wakasema yamejengwa mbali. Naipongeza Serikali na niipongeze sana TAMISEMI kwa kujenga yale masoko na stendi, kwa sababu leo soko kama lile na stendi kama ile, mjini hapa katikati unaweza ukalijenga sehemu gani ukalipata? Kujenga maeneo haya pembezoni mwa miji, maana yake mnakwenda kuutanua mji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu wengi leo wakitaka kununua viwanja katika Dodoma hii, hawawezi kununua huku, wanakwenda kununua Mtumba na maeneo kama hayo. Maana yake ni nini sasa? Mji unakua na watu wanapata fursa. Hapa cha kusaidia ni kwamba, Jiji letu la Dodoma linapaswa viwanja vile vinavyozunguka soko na stendi wagawiwe wananchi wajenge ili lile soko na ile stendi iwe na thamani. Wasifanye tena vile viwanja vikawa ni kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya public. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwapongeze na niwape hongera; tumekwenda Nyamagana kule Ilemela, tumekuta stendi moja ya kisasa sana. Kwa hiyo, kama kuna mpango huu, hata Kondoa tuna uhitaji wa stendi, na tumeisogeza pembeni ili kuukuza mji. Nawaomba sasa Wizara ya TAMISEMI katika maeneo, na tunajua Kondoa ipo katikati ya Manyara na Dodoma. Kondoa ipo karibu na Makao Makuu ya nchi. Kwa maana hiyo, tukipata na ile stendi yetu ambayo tumeiandaa pale pembezeni mwa mji, mtasaidia kukua kwa mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo, ninashukuru sana na ninawapongeza Wizara. Ahsanteni sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi, nishukuru Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa utekelezaji wa Bajeti ambayo hii tunaendelea nayo. Hii inatupa moyo sana na ninaanza kwa kuiunga mkono Bajeti hii mpya ambayo tunakwenda nayo kwa sababu Bajeti iliyopita imetufanyia makubwa na imewatekelezea wananchi kazi kubwa za kimaendeleo kwa maana hiyo ninaanza kwa kuunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Bajeti hii kwenye vipengele vingi lakini hasa hususan hapa kwa kuondoa ada kwenye vyuo vya ufundi kwa kweli umewapunguzia, Serikali imewapunguzia sana mzigo wananchi lakini pia kwa kuweka mikopo katika vyuo vya kati kwa kweli wazazi wamepunguziwa mzigo mkubwa na watoto sasa wana uhakika wa kwenda shule. Kwa hiyo kwa ujumla niipongeze Bajeti ni nzuri na ni ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina baadhi ya ushauri wa mambo ili twende sawa. Katika utekelezaji wa Bajeti iliyopita bado kuna miradi ambayo haijakamilika kwa sababu tofauti tofauti. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Waziri ahakikishe kwamba miradi ile inakamilika, tuangalie vipaumbele vyetu ambavyo tuliviweka halafu tuhakikishe vinakamilika. Mfano miradi ya maji, iko miradi ya maji ambayo inaendelea katika majimbo yetu. Ni vyema ile miradi ya maji tuhakikishe tunapoelekea mwisho huu wa bajeti tuhakikishe ile miradi inawekewa mipango mizuri ya kukamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi ya maji wakandarasi wamekuwa ni dhaifu sana, wamekuwa hawana uwezo na hata wakipewa fedha na Serikali wanakimbia kimbia. Sasa sijajua hii miradi ambayo wakandarasi wamepewa hela na Serikali wanakuwa na visingizio. Mfano kuna miradi miwili ya maji visingizio vikubwa vinakuwa ni ukosefu wa mabomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi hii inachukua muda mrefu sana. Mradi wa shilingi milioni 800 unatekelezwa toka Bajeti ya mwaka wa kwanza, mwaka wa pili na mwaka huu unakwenda ni wa tatu lakini Bajeti hiyo inaendelea kutekelezwa, kutekelezwa mpaka sisi sasa wawakilishi wa wananchi tunashindwa kwenda kufanya mikutano kule kwa sababu kila siku ukienda hadithi ni hiyo hiyo. Kwa hiyo, nataka hili hebu lifanyiwe kazi na liishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano pale kwetu kuna wakandarasi wawili walipewa hela na Serikali lakini visingizio mwaka mzima mabomba hakuna. Sasa kama mabomba hakuna lazima Serikali ione namna ya kuikwamua hii miradi ili wananchi waanze kufikiria miradi mingine. Lakini miradi mingine kama mradi ule wa mjini tunaishukuru Serikali juzi imetoa shilingi milioni 600, certificate ya yule mkandarasi na amepata matumaini ya kuendelea na mradi. Mradi uko 72% na zaidi lakini alikwama kwa sababu fedha zilichelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba miradi hii ambayo ni muhimu sana, ni miradi ya kimkakati ambayo Mheshimiwa Rais ameweka ahadi ya kuwatua ndoo wakina mama kichwani tuiangalie lakini miradi mingine ni miradi ile ya visima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na Bajeti mwaka wa kwanza, mwaka wa pili na huu ni mwaka wa tatu. Mwaka wa kwanza tunachimba visima, mwaka wa pili tunafanya feasibility study, mwaka wa tatu ndiyo tunaanza usambazaji. Jambo hili linatukatisha tamaa, ni bora miradi hii yenyewe siyo gharama kubwa sana. Mradi wa kuchimba kisima na kusambaza kwenye mitaa yetu yawezekana shilingi milioni 150.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nashauri Serikali inapokuja na miradi ya namna hii ya muhimu ya maji basi ije na mradi uliokamilika, wachimbe kisima kwa wakati huo huo wakati wana chimba kisima, basi wataalamu wawe wameshafanyia feasibility study ili waanze kusambaza kuliko kisima kinakaa mika mitatu hakijapelekewa fedha za usambazaji. Kwa maana hiyo tuna visima zaidi ya 10 kwenye Jimbo la Kondoa Mjini vinahitaji usambazaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, safari hii kwa Bajeti hii tutachimba tena visima vingine, vile vya mwanzo hatujavisambaza. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri Serikali hebu iangalie miradi yote ambayo tayari imekwisha peleka fedha nyingi basi tuimalizie kwa kuikamilisha ili iweze kuanza kutumika na tuanze kubuni miradi mingine kwa ajili ya kuwasaidia wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo jingine la kukumbusha. Ilani ya CCM bado nazungumzia Barabara inayotoka Tanga kuja Mrijo kwenda Kwa Mtoro kwenda Singida. Ninaamini Dkt. Samia Suluhu Hassan ambaye ndiyo Mwenyekiti wa CCM anaifahamu barabara hii ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na imetamkwa vizuri sana itatoka Mondo itakuja Mpaka Bicha. Sasa tumeweka juzi tulihudhuria sherehe ya kusaini mkataba wa hiyo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika matamko ya Mheshimiwa Waziri kile kipande hakijatajwa. Ninashukuru kwenye Hotuba ya Bajeti kipo nimekiona. Kwa hiyo, nadhani Serikali izingatie ule Mpango uliopo kwenye Ilani ya CCM kwa maana hiyo ninaomba wakati tuanendelea kujenga ile barabara tujue kabisa barabara iliyotajwa kwenye Ilani ya CCM inatoka Mondo kuja Bicha na yenyewe izingatiwe katika hii hatua hii ambayo tumesaini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tumekuwa tukizungumza mara kwa mara hili Daraja la Munguri B. Ni muhimu sana daraja hili likajengwa mapema kwa sababu sisi Wanakondoa na Watu wa Hanang’ tunalitegemea sana kwenye shughuli za uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi alikuwepo Katibu Mkuu wa CCM Ndugu Daniel Chongolo katika Jimbo langu kuzungumzia na alimwita mtaalamu kuzungumzia. Sababu ambazo zinatolewa haziridhishi kusema kwamba daraja lile lisijengwe. Wamekwenda kufanya feasibility study kwenye eneo refu la mita 500 wakati daraja la awali lilikuwepo mita 100 ambalo linaweza likatumia fedha ndogo ambayo walikuwa wanaangalia kwamba economic not viable wakashindwa kulijenga kwenye hiyo mita 500 ilitakiwa wale wataalamu wangeenda kuchukua vipimo kwenye eneo la zamani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapa lazima wataingia gharama mara mbili. Wamekwenda kufanya uchunguzi lakini wamekwenda wamekuja na matokeo ambayo Serikali wanasema haiwezi kujenga daraja kwenye eneo lile ni refu wanatakiwa waanze tena upya kuja kupima kwenye eneo la zamani ambalo ni mita 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashangaa kwa nini kwa gharama ile ile wasingepima kule pafupi ili wafupishe huu mlolongo mrefu wa kujenga hiyo daraja? Daraja hiyo inapoteza magari ya watu yanazama, watu wana umia, watu wanaingia gharama kuvushwa kwenye daraja lile hata kama haifai kiuchumi lakini Serikali yetu lazima ijue maeneo yale ni maeneo ya wananchi na wananchi wanaingiza vipato kwa kilimo ng’ambo ya pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekwishapeleka fedha eneo lile kwenye Pori la Swagaswaga. Wamejenga mageti, wamejenga hosteli unasemaje sasa tena kiuchumi haifai wakati tayari umekwishapeleka fedha upande ule? Kwa hiyo, lile daraja likijengwa hata hao watalii ndiyo watapita, vinginevyo masika yote hata kama tutakuwa na watalii hawawezi kupita kwa sababu daraja linapitisha maji na mto unapitisha maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Wizara ya Ujenzi ichukulie serious ujenzi wa daraja hili ambalo linaunganisha mikoa miwili Dodoma pamoja na Mkoa wa Manyara. Kwa hiyo nilikuwa nakumbusha hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na ujenzi wa sekondari unaendelea huu wa mradi wa SEQUIP, tulikuwa na ile awamu ya kwanza tunashukuru Serikali ilituletea fedha. Jimboni kwangu tumekamilisha ile sekondari na leo wanafunzi wanasoma kidato cha kwanza na kidato cha pili, tunasubiria basi ile awamu nyingine ya pili. Na sasa hivi halmashauri ndio hivyo zinakwenda kufungiwa yao tunakwenda kumaliza. Sina uhakika kwamba hizo fedha zitakuja katika kipindii hiki kabla mwaka wa bajeti haujaisha ama tutatarajia zitakuja kwa mwaka mwingine unaofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatakiwa tujenge sekondari nyingine hiyo Kata ya Bolisa ambayo miaka mingi wamekuwa wakisubiri kata yao wanakwenda kusoma kata nyingine. Kwa hiyo tunataka tujue sasa ile fedha itaingia sasa au tutaivusha kwenda kwenye bajeti? Na kama tukiiivusha mwaka unaofuata sekondari tutajenga nyingine? Kwa hiyo nilitaka nifahamu hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kufanya kazi nzuri ya uhifadhi. Leo ukiona Waheshimiwa Wabunge wote wanalalamika tembo wamekuwa wengi maana yake Wizara imefanya kazi kubwa ya kuwalinda hao tembo ambao walikuwa wanakwenda kupotea kutokana na majangili. Tunawapongeza sana Wizara ya Maliasili na Utalii kwa namna walivyoweza kulinda hifadhi zetu mpaka leo sisi Wabunge wote takriban, maeneo mengi tunalalamika tembo wamekuwa ni kero maana yake kazi yao wameifanya vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kinachotakiwa kufanyika ni lazima sasa ipangike mikakati kama Serikali tumeweza kupanga mikakati mizuri ya kuhifadhi hifadhi zetu wanyama wetu leo wameongezeka basi wasije wakawa tena kero kwa wananchi. Bajeti hizi zinatakiwa zizingatie mambo haya. Kwamba tumeweza kuhifadhi sasa, tembo wamekuwa wengi ni namna gani tunaweza kuwadhibiti tena isiwe ni dhahma kwa wananchi. Maeneo mengi na Serikali inatumia fedha nyingi sana kwenda kulipa vifuta jasho na vifuta machozi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa kwenye jimbo la dada yangu Dkt. Ashatu Kijaji juzi wakati wa Katibu Mkuu, mwananchi anaongea kana kwamba sasa anajua kabisa anakwenda kulima, nikishalima tembo watakuja kula Serikali ijiandae kulipa kifutamachozi sio sawa. Kwa sababu kifutamachozi chenyewe kinachotoka tunafahamu wote hakitoshi. Mtu analima heka kumi analipwa hela za kununua gunia mbili; hii haifai. Kwa hiyo Serikali iweke mikakati mizuri ya kuwadhibiti hawa tembo kwa sababu wamekuwa waharibifu. Ikiwezekana kama wanauzika watangaze soko, wawauze tembo kwa mwenye kuwataka ili wapungue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo nashukuru sana ninaomba kuwasilisha na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, nimshukuru Mwenyezi Mungu, lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niishukuru Serikali ya Awamu ya Tano, chini ya Dokta John Joseph Pombe Magufuli, Mama Samia na Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa. Pia nitoe shukrani kwa Mawaziri wa Awamu iliyopita kwa kazi kubwa waliyomsaidia Rais wa nchi katika kutekeleza shughuli mbalimbali katika nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mambo mazuri yaliyofanyika awamu iliyopita, pia mimi mchango wangu katika mpango huu ni kama ifuatavyo, moja nitagusa sehemu ya kilimo. Kama tunataka tufikie malengo ya kilimo katika nchi yetu ni lazima kwanza mambo yafuatayo yafanyike. Moja, tuhakikishe ile migogoro mikubwa ya mashamba kati ya wananchi na taasisi za Serikali inamalizwa mapema ili kutoa nafasi kwa wananchi kuendelea kufanya kilimo. Iko migogoro kati ya wananchi na Jeshi la Magereza kuhusiana na mashamba na imechukua muda mrefu kiasi ambacho imekuwa ikisimamisha shughuli za kilimo kwa wananchi hasa maeneo ya Kingale kwa kule kwetu Kondoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili tujikite katika mbegu. Soko la jana nilikwenda katika maduka ya mbegu, mfuko wa kilo mbili wa alizeti unauzwa kati ya Sh.15,000 mpaka Sh.16,000. Kwa hiyo, Mpango ungejiwekeza katika maeneo ya uandaaji wa mbegu ili kurahisisha upatikanaji wa mbegu kwa bei nafuu kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni kuhusu viwanda. Tumekuwa na viwanda vingi sana katika nchi hii. Nimekuwa Mkoa wa Pwani, tumekuwa tukiuita Mkoa wa Viwanda kwa sababu viko viwanda ambavyo vinaonekana, ni kazi kubwa iliyofanyika katika Serikali hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la nne, Mpango huu unatakiwa uendane sambamba na kuweka tahadhari ya kuilinda miundombinu pamoja na mali za wenye viwanda. Nimewahi kushuhudia kiwanda kinaungua moto mpaka kinamalizika hakuna zimamoto. Kwa hiyo, nashauri kwenye Mpango huu wakati tunaandaa mipango ya viwanda tujaribu na Wizara nyingine ziwe zinashirikiana katika kufanya ulinzi. Kiwanda cha Mafuta ya Alizeti Kondoa kiliungua mpaka kikamalizika hakuna zimamoto. Walipofanya juhudi ya kutafuta zimamoto Babati, Manyara, zimamoto linapatikana kiwanda kimeungua mpaka kimeisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia wawekezaji wa mabasi, muda mfupi badaye basi la abiria pia likaungua mpaka linamalizika, hakuna zimamoto. Kwa hiyo, tunaomba katika Mpango huu pia, Wizara ya Ulinzi iangalie maeneo yale ambayo yanakosa zimamoto yatufanyie mpango wa kupata zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tano, Mpango huu tunaomba uimarishe uwajibikaji, uadilifu na uaminifu katika sekta zote ambazo watu wamepewa majukumu ya kumsaidia Mheshimiwa Rais ikiwepo kwenye eneo la TRA. Bado kuna mianya mingi sana ya kodi kupotea na yako maeneo mengi kabisa kodi hazilipwi. Kwa hiyo, Mpango huu uendelee kuweka mkakati kwa ajili ya kuhakikisha kodi ya Serikali inaingia hasa kwa kutumia zaidi TEHAMA katika ukusanyaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii lakini niwapongeze Mheshimiwa Jafo na Mheshimiwa Chande kwa wasilisho lililo zuri kabisa kwenye bajeti yao. Nilikuwa naomba nichangie eneo dogo la mazingira wewe unafahamu mji wa Kondoa umekatiza mto mkubwa pale, sasa mto ule umehama kutoka njia yake ya asili kwenda mto mkondo mdogo.

Mheshimiwa Spika, huu ni msimu wa pili madhara yanayotokea kwenye mto ule ni makubwa sana nilikuwa naomba Wizara iweke fungu kwa ajili ya kuurudisha ule mto kwenye mkondo wake wa asili. Kwasababu madhara ambayo yanatokea kwa hivi sasa kwanza maji ni mengi yana-force kuingia kwenye mkondo mdogo, mashamba ya watu yanaendelea kumegwa na maji yanaelekea kwenye nyumba za watu, kama hatujaudhibiti kwa kwa wakati mto ule maeneo ambayo yanakwenda kuathirika ni pamoja na shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shule ya msingi Mpalangwi eneo lote la kanisa la Katholic makaburi yaliyopo kule pamoja na Chuo cha Bustani, kwasababu mto wenyewe ule ni mdogo sana maji yanatafuta njia mbadala ya kupita, kwa sasa kwasababu ni mkondo mdogo maji yanaingia mashambani yanakwenda kuharibu mazao ya wananchi. Lakini sio hiyo tu miundombinu ya TANESCO pia ipo mashakani kwasababu zipo nguzo ambazo tayari na zenyewe zimekwisha kufikiwa na maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba watenge fedha kwa ajili ya kurejesha ule mto katika chanzo chake cha asili. Aidha, Mheshimiwa Waziri aagize watu wa NEMC waende wakafanye tathmini mapema ili kuweza kuurejesha ule mto katika chanzo chake cha asili. Hasara nyingine inayojitokeza barabara ile inayotoka Iboni kuelekea Bolisa mpaka Gubali inakuwa haipitiki kwasababu Serikali itakuja kuingia gharama kubwa ya kujenga madaraja makubwa.

Mheshimiwa Spika, msimu wa mvua uliopita daraja ambalo lilijengwa na gharama kubwa na Serikali lilisombwa na maji zima zima kama lilivyo likahamishwa zaidi ya mita 200, kwa hiyo, pale fedha ya Serikali ilipotea kabla daraja halikuanza kujengwa, ni kwasababu ya nguvu ya maji ambayo ilikuwa inatoka kwenye mto mkubwa kwenda kwenye mto mdogo. Nilikuwa naomba tu eneo hili ili kuokoa hata shughuli za kiuchumi za wananchi wa kata ya Kondoa Mjini na Kata ya Bolisa kuelekea kata ya Kolo Gubadi zile barabara ili ziwe salama inabidi mto huu urejeshwe kwenye mkondo wake wa asili.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo ninakushukuru sana kwa nafasi hii ahsante sana naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALI J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Wizara lakini pia mimi nichangie katika eneo la elimu. Niikumbushe Wizara ya TAMISEMI kwamba Serikali ilichukua Shule ya Wasichana ya Kondoa na kuifanya shule ya Advanced Level na hivyo ikawa ni shule ya kidato cha tano na cha sita, lakini shule ile ilikuwa ni ya O-Level. Baada ya Serikali kuibadilisha hatukupata tena sekondari ya bweni ya wasichana ya Kondoa. Kwa hiyo, naomba katika mpango wa Wizara wa ujenzi wa sekondari kumi za bweni za wasichana, basi waende wakaifidie ile sekondari katika Jimbo la Kondoa Mjini ili mabinti zetu wa kidato cha kwanza hadi cha nne waweze kuendelea kupata masomo katika mazingira mazuri.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa elimu, tuna shule yetu shikizi ambayo sasa hivi imekwisha mature. Shule ile wananchi walijenga, sasa tuna madarasa manne, wako wanafunzi 300 ina mwalimu mmoja. Kwa hiyo, naiomba Wizara watusaidie kujenga majengo matatu ikamilishe majengo saba ili wanafunzi wale waendelee kusoma na isajiliwe iwe shule kamili ya msingi. Tukisema kuwarudisha katika shule mama itakuwa ni vigumu kutokana na mazingira magumu na umbali wa kutoka Chang’ombe hadi shule mama ilipo eneo la Tumbelo.

Mheshimiwa Spika, naishauri na kuiiomba Serikali kwamba walimu waliojitolea ni wengi, basi walimu wale katika ajira hizi wapewe kipaumbele kwa sababu wametumia muda wao mwingi kujitolea kufundisha katika sekondari hizo. Pia nishauri, wapo vijana wengi waliomaliza masomo ya ualimu, hawana kazi wako mitaani wakati Serikali inafanya mpango wa kuwaajiri basi watoe tamko la wale vijana waendelee kwenda kuzisaidia shule zetu kwa kujitolea angalau wawekewe fungu hata la kupata fedha ya nauli na sabuni kwa ajili ya kujikimu.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa afya, tunafahamu Hospitali yetu ya Wilaya ya Kondoa ilijengwa miaka mingi sana. Leo vituo vya afya vinavyojengwa kwenye kata ni bora kuliko Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa, ni hospitali kongwe sana. Naomba sasa katika ule mpango wa Wizara wa kujenga hospitali mpya, wafikirie namna gani sasa ya kupeleka fedha pia Kondoa kwa ajili ya kujenga hospitali mpya ukizingatia sasa Kondoa ni Halmashauri ya Mji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga barabara nzuri sana Kondoa, kwa hiyo, mazingira ya barabara ile yanavutia ajali nyingi. Mara nyingi zinatokea ajali, majeruhi wanapopelekwa kwenye hospitali ile wanakosa huduma na hivyo wanapewa transfer kuja Dodoma. Wakati huohuo, hospitali ya mji haina hata ambulance, kwa hiyo, wanaanza kuhangaika kutafuta ambulance kuwaleta watu Dodoma. Kwa hiyo, naomba mambo mawili hayo kwamba katika mpango wao waweze kusaidia kuijenga Hospitali ya Halmashauri ya Mji lakini pia basi wapeleke ambulance kwa ajili ya kusaidia watu wanapotakiwa kupewa transfer. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo linguine kwenye hospitali hii tunayo X-ray ya kisasa kabisa lakini watu wanakwenda kupimwa pale wanapewa CD wanakuja kusomewa majibu Dodoma. Tunaomba basi papelekwe mtaalam kwa ajili ya kurahisisha utoaji wa huduma hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha ajabu zaidi ni kwamba hospitali kongwe haina chumba cha maiti. Juzi imetokea ajali watu karibu nane wamefariki lakini hatuna mortuary. Kwa hiyo, tunaomba watusaidie kujenga mortuary kwa ajili ya kuhifadhi maiti wetu.

Mheshimiwa Spika, katika upande wa miundombinu, matatizo ni kama yalivyo katika Halmashauri nyingine; barabara zetu ni mbovu. Tulikuwa tunaomba, Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Kondoa itenganishwe wapatikane Mameneja wawili wa TANROADS ili mmoja afanyie upande wa Kondoa DC na mwingine Kondoa Mjini ili kuwapunguzia mzigo maana eneo ni kubwa sana. Izingatiwe Kondoa ni kubwa imetoa wilaya mbili na majimbo matatu. Kwa hiyo, ni wilaya kubwa sana, tunaomba tupate Meneja wa tofauti kati ya Wilaya ya Kondoa na Kondoa Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa wakati huu. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii na Kamati ya Kudumu Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu shughuli za Kamati hizo kwa Mwaka 2021
MHE. ALLY J. MAKOA – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA UTALII:
Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuhitimisha hoja. Nawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa michango yao mizuri ambayo kwa kweli imezidi kutuimarisha na ninadhani Serikali imesikia. Ninawashukuru Mawaziri waliochangia lakini kipekee kabisa nimshukuru Waziri Mkuu kwa maelekezo yake mazuri ambayo ameyatoa hapa mbele ya Bunge, ni matumaini ya Kamati kwamba sasa Serikali itakwenda kuyafanyia kazi mawazo ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, pamekuwa na hisia kubwa sana kwa upande wa Ngorongoro lakini lazima na Bonde la Kilombero na lenyewe litiliwe mkazo kama jinsi ambavyo Ngorongoro inavyotiliwa mkazo kwa sababu Bonde lile na lenyewe likiachiwa yatakuja kutokea madhara makubwa pengine kama haya yanayoweza kutokea Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, sasa ninaomba kutoa hoja kwamba Bunge likubali kupoipokea taarifa yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kutoa hoja. (Makofi)

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu lakini niwapongeze Waziri wa Ardhi, Naibu Waziri, Katibu Mkuu na hata Kamishna Mkuu wa Ardhi kwa kazi kubwa wanazozifanya. Pia nisiwe mchoyo wa fadhila kumpongeza Kamishna wa Mkoa ndugu yangu Kabonge kwa majukumu makubwa anayohudumia Mkoa wa Dodoma, katika kuhakikisha wananchi wanapata hati.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, niendelee na mchango wangu kwamba ardhi ni bidhaa pekee ambayo kama tutaitumia vizuri Taifa letu litaendelea kupata kipato endelevu. Ni kipato ambacho hakiyumbi kwa sababu hatutegemei kwamba kuna mwaka mapato yanayotokana na ardhi yatapungua kwa sababu kila mwaka tunapima ardhi na watu wanaendelea kulipa kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni chanzo pekee cha uhakika cha mapato ya Taifa letu ni lazima sasa kuiwekea miundombinu rafiki Wizara hii ili kuhakikisha mapato yanayotokana na ardhi kila mwaka yanaendelea kupanda. Nyenzo mojawapo ni kusaidia Wizara hii kupata watumishi wa kutosha katika zoezi la kuhakikisha kwamba upimaji wa ardhi unafanyika kwa ufanisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri nyingi hazina Maafisa wa Ardhi. Unakuta halmashauri ina afisa mmoja huyo ndio apime, huyo ndio aandae ramani, maana yake utagundua kwamba hatuwezi kufikia malengo ya upimaji wa ardhi kama tunavyohitaji. Kwa hiyo Serikali iangalie, katika ajira ni vyema kuipa kipaumbele Wizara ya Ardhi kuajiri watendaji wa ardhi ili kuhakikisha kwamba zoezi hili la upimaji linakwenda kikamilifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja iliyo Mezani ni ardhi. Watanzania wengi vipato vyao ni vya chini sana. Mifumo ambayo inatumika kumilikisha ardhi ni mifumo ambayo si rafiki kwa Watanzania wengi ambao vipato vyao ni vya chini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, naweza nikasema kwamba, ardhi inaweza ikawa inauzwa milioni nne kwa kima cha chini na mnunuzi anatakiwa alipe kwa muda mfupi sana; miezi mitatu. Unajiuliza, ni Mtanzania wa aina gani huyu ambaye amelengwa kununua ardhi kwa bei kubwa kiasi hicho, hali ya kuwa kipato chao ni kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa nashauri sasa Wizara ya Ardhi ikishirikiana na TAMISEMI, kwa maana ya halmashauri, watafute miundombinu, watafute njia rahisi za kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anamiliki ardhi kutokana na kipato chake alichonacho. Wanaweza wakaenda kupata wawekezaji. Mfano, wanaweza kuingia kwenye mabenki wakawa wanatoa hati, hati zinakwenda benki, Watanzania wenye kipato cha chini kidogo wakawa wanagomboa hati zao mabenki kwa kipindi hata cha miaka mitatu mpaka mitano, lakini kwa miezi mitatu Watanzania wachache sana wataweza kumiliki ardhi. Nina ushahidi; vijana wengi wamerudisha ardhi baada ya kushindwa kukamilisha malipo kwa sababu wameshindwa kutekeleza mkataba walioingia wa kulipa ardhi kwa kipindi cha miezi mitatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hilo la wananchi wengi kushindwa kununua ardhi linakwamisha mapato ya ardhi kwa sababu kama ardhi hainunuliwi maana yake hati hazitaandaliwa. Kama hati hazitaandaliwa maana yake Serikali itapoteza fedha nyingi kutokana na hati, lakini kama hati nyingi zitanunuliwa, Serikali itapata fedha nyingi sana. Kwa hiyo tuweke mfumo rahisi wa wananchi kupata hati mapema. Ikiwezekana, wananchi wauziwe hati na siyo wauziwe maeneo. Maandalizi ya hati yatangulie halafu ndipo watu watangaziwe kuuziwa viwanja ambavyo tayari vimekamilika hati. Hapo Ardhi itaendelea kupata fedha kupitia hati zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na migogoro; nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri, wanashughulika kikamilifu sana kutatua migogoro ya ardhi. Sasa pale kwetu, nilizungumza na Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna migogoro mitatu ambayo inawasubiri wao tu ili iweze kukamilika. Hapa nimekubaliana na usemi wake wa kusema kwamba, maeneo yote ya wananchi yaliyochukuliwa hayakulipwa fidia, warejeshewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tuna mgogoro ambao upo baina ya wananchi na halmashauri na wamiliki. Halmashauri imechukua maeneo ya mtu, ya wananchi, haikulipa fidia. Lakini imeyapima yale maeneo na maeneo yamekwishauzwa kwa wananchi na wananchi wamekwishalipa fedha zao. Sasa wananchi wenye maeneo hawakulipwa fidia, wamezuia shughuli yoyote ya maendeleo kama matamko ya Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo namwomba ile nia yake ya kwenda Kondoa kwa ajili ya kusaidia kutatua huu mgogoro kila mmoja apate haki yake, aendelee kuwa nao. Naomba baada ya zoezi hili tufuatane naye kwa ajili ya kwenda kutatua mgogoro huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, upo mgogoro mwingine wa ardhi wa wananchi, kijiji pamoja na Hifadhi ya Swagaswaga. Wananchi wa Mongoroma na maeneo yanayopitiwa na hifadhi ile wao wanalalamikia mipaka. Najua siku atakayokuja Waziri, tutakwenda kutembea na kuwasikiliza wale wananchi. Zoezi hili la migogoro ya ardhi inayohusiana na mipaka ni matumaini yangu kwamba tutakwenda kulimaliza kama tutafika kwa wananchi kuwasikiliza halafu sisi wenye mamlaka, Mheshimiwa Waziri, viongozi pamoja na wananchi na mimi Mwakilishi wao, tukae tuone namna gani tunakwenda kuitatua hii migogoro ili wananchi waendelee na shughuli za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro namba tatu upo kati ya wananchi wa Iyoli na maeneo yanayohusiana na mgogoro Kata ya Kingale kati ya wananchi na Magereza. Waliotoa viwanja kukaribisha Gereza la King’ang’a wapo. Wenye kumiliki gereza hilo wapo. Viongozi tupo na sisi wawakilishi pia tupo; tunashindwaje kwenda kumaliza mgogoro huu ili wananchi waendelee na shughuli za kilimo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nina matumaini makubwa sana. Ahadi ya Waziri ya kwenda Kondoa kumaliza migogoro hii ikikamilika wananchi watakwenda kufanya shughuli zao za kujiongezea kipato na migogoro hii ambayo inaendelea itakuwa imekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia huu mchango. Awali ya yote mimi nimpongeze Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kukamilisha zoezi la Sensa ya Watu na Makazi, kwa sababu zoezi hili litatufanya sasa sisi Wasaidizi wake na Viongozi kuweza kutumia vizuri takwimu za watu katika kuhakikisha tunapanga maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye maeneo matatu. Kwanza kwenye sekta ya ardhi. Kutokana na ukuaji wa idadi ya watu kama tulivyoona kwenye taarifa ya sensa, tunagundua kwamba tumeweza kuongezeka kutoka miaka 10 iliyopita kwa asilimia Tatu. Watu wameongezeka kwa idadi ya zaidi Milioni 16.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama watu wameongezeka kwa kiasi hiki ni lazima Taifa tuweze kuweka mpango mzuri wa kuhakikisha kwamba mipango ya ardhi inawekwa sawa kwa ajili ya matumizi ya leo na kesho. Kama hatukuweka mipango mizuri ya matumizi ya ardhi leo, huko tunapokwenda kutakuwa na vurugu na migogoro mingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mpango huu, ninashauri kwamba mpango ujikite sana katika kuiwezesha Wizara ya Ardhi hasa kule kwenye Tume ya Mipango ili iweze kuongeza kasi ya ukuaji wa upimaji wa viwanja na maeneo ili kuweza kupanga Watanzania na kuondoa migogoro. Leo migogoro mingi inasababishwa na eneo kubwa la nchi yetu kutokupimwa na kupangwa. Kwa hiyo, napendekeza mpango uweke nguvu kubwa katika Wizara ya Ardhi hasa kule kwenye Tume ya Mipango ya Ardhi ili tuweze kufanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kwenye sekta ya maliasili. Leo utaona wananchi wengi na Waheshimiwa Wabunge, wakilalamika kuhusiana na migogoro baina ya wanyama na wanadamu. Sasa kutokana na hilo, iko haja sasa mpango wetu ukajikita sana katika kuhakikisha wanaiwezesha Wizara ya Maliasili katika kuhakikisha kwamba wanakabiliana na majanga kama hayo. Tunapaswa kupanga mipango na tunapaswa kuiwezesha Wizara, kiwango kile ambacho kinaweza kunufaisha Taifa. Mfano, leo Wizara ya Maliasili inachangia asilimia 17 kwenye Pato la Taifa, lakini kiuhalisia ukiangalia vyanzo vya utalii vilivyomo katika nchi haviendani na kiwango cha mchango wa Pato la Taifa la asilimia 17. Hivyo tunataka tuone kwamba tunaweka mipango thabiti kuhakikisha kipato kinachochangiwa na sekta hii ya utalii kinaongezeka kulingana na ukubwa wa vyanzo vyetu vya utalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaliwezaje hili? Ni pale Serikali itakapokuwa tayari sasa kuhakikisha wanaweka nguvu kwenye sekta hii. Serikali imefanya vizuri sana katika kuiwezesha Wizara ya Maliasili. Mfano, wamegaiwa magari ya kuweka miundombinu katika mbuga zetu na hifadhi mbalimbali. Je, baada ya mradi ule kuisha, yale magari tunaweza kuyaendesha vizuri yakaendelea kukaa muda mrefu katika maeneo yetu ama kwa ukosefu wa bajeti inawezekana magari yale yakaharibika muda mrefu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano, TANAPA mwanzo ilikuwa inasimamia hifadhi 16, bajeti yao ilikuwa ni Shilingi Bilioni 100. Miaka kadhaa baadae ikaongezewa hifadhi nyingine kufikia hifadhi 22, lakini bajeti ilibaki vilevile. Zoezi la kusimamia hifadhi hizi kwa vyovyote lazima litakuwa ni gumu kwa sababu wameongezewa idadi ya maeneo. Mfano, mwanzo walikuwa na kilometa za mraba 57,333, wameongezewa kilometa za mraba 47,471 lakini bajeti katika kipindi cha miaka mitatu imebaki hiyo hiyo Bilioni 100. Kwa hiyo, ili tuweze kuwasaidia watu hawa wa maliasili waweze kukabiliana na tembo na wanyama waharibifu lazima tuone uwezekano wa kuisaidia Wizara hii ili kuondoa migogoro baina ya wanyama pamoja na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia migogoro ya ardhi baina ya hifadhi na vijiji. Mheshimiwa Rais ametuma Kamati ya Mawaziri Nane katika kuhakikisha wanatatua migogoro. Sasa sijajua huko maeneo mengine lakini juzi mimi nilihudhuria kwenye kikao kimoja cha utatuzi, nilichokigundua, kama Mawaziri Nane hawajachukua lile jukumu lao kikamilifu, wakawaachia watu wa ngazi za Wilaya, migogoro hii haitaisha na itaendelea kuwa mikubwa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawatasimamia wenyewe wakawaachia kule Wilayani, tutajikuta kwamba migogoro hii haitaisha. Mfano, nimepokea taarifa ya Halmashauri mbili, Halmashauri ya Chemba na Halmashauri ya Kondoa na Halmashauri ya Mji, mapendekezo yaliyotoka Wilayani yana-double standard. Mfano wanatoa kaya 411 zote zitoke halafu hazielekezwi kaya hizo zenye watu zaidi ya 1,700 waende wapi. Taarifa inasema waende kwenye Kijiji Mama. Ukienda kwenye Kijiji Mama unakuta kila mmoja ana eneo lake. Sasa kaya hizi kwa taarifa nyepesi nyepesi kama hizi itakuwa hatusaidii badala ya kutatua mgogoro, tutazalisha migogoro mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo bado ninatoa rai kwa Serikali iweze kulisimamia hili vizuri ili kuhakikisha inatatuliwa kwa sababu migogoro pia inakwamisha mipango ya Serikali hasa kwa mtu mmoja mmoja na uchumi wa nchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye sekta ya uchukuzi. Nilizungumza Bunge lililopita hapa. Barabara hii ya Handeni ambayo nimeikuta pia hapa kwenye mpango huu. Kwa sababu Ilani ya CCM ilitaja barabara hii lazima ifike Kondoa halafu utekelezaji inapitia Chemba. Kwa sababu mipango yote, mpango wa miaka mitano na mpango huu ulielezea barabara hii ipitie kule, basi Serikali ikumbuke jambo hili. Mpango ule wa awali na Ilani inavyosema barabara hii ipitie Kondoa, halafu hii barabara mpya waliyoichonga waiingize kwenye Mpango huu ili na yenyewe iwe inatekelezwa kwa mujibu wa Mpango na Ilani ya CCM.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyaseama hayo, ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE ALLY J. MAKOA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA ARDHI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi tena ya kuja kumalizia hoja yangu. Kabla ya hapo, nawashukuru sana Waheshimiwa Wabunge ambao wamepata nafasi ya kuchangia kwenye hoja ya Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Tulipata Wabunge 11 ambao walichangia hoja yetu. Ninawashukuru sana kwa michango mizuri na nimeona michango mingi imeendana na mapendekezo na ushauri wa Kamati ambapo Kamati yangu ya Ardhi, Maliasili na Utalii imetoa kwa Serikali.

Mheshimiwa mwenyekiti, mambo machache tu ya kufafanua. Unajua kama Kamati tuliona deal la Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kama limekubali vile baada ya programme ya Royal Tour na ndiyo ikapelekea kushauri baadhi ya mambo katika Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajumbe wengi wamechangia kuhusiana na taasisi hizi za Wizara ya Maliasili, TANAPA, TAWA na NCAA Mamlaka ya Ngorongoro kwamba ziongezewe fedha ili ziweze kufanya majukumu yao kulingana na hali ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano tu kwamba TANAPA Bunge hili liliweka lengo la kukusanya shilingi bilioni 257.5 kwenye bajeti lakini wakati tunapitia utekelezaji wa bajeti TANAPA mpaka kipindi cha December ilikuwa imeshakusanya shilingi 2,051,000,000 ambayo ni sawa na asilimia 97 ya tengo lote. TAWA walikuwa na lengo la kukusanya shilingi bilioni 63.8 lakini mpaka kufikia kipindi hiki cha nusu mwaka wameweza kukusanya kwa asilimia 62. Ngorongoro walikuwa wana shilingi bilioni 148, hadi kufikia nusu mwaka wamekusanya shilingi bilioni 98.5 ambayo ni sawa na asilimia 66.6.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeyasikia maneno ya Mheshimiwa Dkt. Mwigulu hapa kwamba ukitaka kuvuna lazima upande. Ndiyo maana ile ile kwamba tunasisitiza Serikali izihudumie vizuri hizi taasisi ili ziweze kufikia malengo ambayo Mheshimiwa Rais anayategemea. Ndiyo maana yeye mwenyewe ameamua kujitoa katika kuhakikisha Wizara hii inatoa mchango unaostahiki kulingana na hifadhi zote na nyingi tulizonazo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wajumbe wamezungumzia pia suala la mkopo wa Shilingi bilioni 345. Kamati iliona iko haja ya malengo yale yale yaliyowekwa na Wizara ya kuboresha mfumo wa ILMIS pamoja na kuimarisha mpango wa ardhi. Kamati iliangalia kwa undani sana suala hili na iliweza kupata maelezo kutoka Wizarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Kamati tuliona, kama tungeweza kuongeza upangaji wa vijiji, maana yake tungekuwa na faida ya kwamba kwanza tutaondoa migogoro katika nchi hii; na pili, tutaboresha data base za Wizara katika kila Mkoa kama maeneo yetu yatapimwa; tatu, tutakuwa tumetekeleza ilani ya Chama cha Mapinduzi; nne, tutakuwa tumetimiza Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano; tano, itajibu maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoweza kuyatoa katika Bunge hili kwamba, Wizara ya Ardhi ihakikishe kwamba inapanga matumizi bora ya ardhi nchi nzima ili kurahisisha na kuondoa urasimu kwa wawekezaji wanapokuja nchini kuwekeza katika sekta ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, haya yote tuliyaona na tukaona ni muhimu sana. Hata kama Wizara ingeamua kuvipima vijiji vyote ambavyo vilibaki, pesa ambayo ingetumika ni Shilingi bilioni 145, ambapo Wizara ingebaki na Shilingi bilioni 200 ambayo ingeweza kupangia majukumu mengine ya kuimarisha mfumo na vitu kama hivyo. Haya yalikuwa ni mawazo tu ya Kamati na ndiyo tumeyaleta mbele ya Bunge lako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaiomba Serikali iendelee kuangalia haya mapendekezo ili kuweza kufikia malengo ya kuipima nchi yetu yote ili kuondokana na migogoro ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, nakushukuru tena wewe na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge na sasa ninaomba kutoa hoja.

MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, naafiki.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara iimarishe shughuli za Jeshi la Magereza hususani Gereza la King'ang'a kwa kufanya mambo yafuatayo; kwanza, kupima eneo la gereza lote na kupata hatimiliki ili kuepuka uvamizi wa eneo hilo na kulipangia matumizi bora ya ardhi.

Pili, kuwe na ufugaji wenye tija kuliko ilivyo sasa kuna kundi kubwa la ng'ombe lenye tija ndogo sana. Wanafuga kienyeji, hawana shamba la malisho, hawana kisima cha maji, hawana josho la koushea mifugo, hawana wataalam wa kusimamia mifugo matokeo yake hata product ya mifugo yao ni kilo chache sana. Wananchi hawana cha kujifunza kutoka Gereza la Mifugo King'ang'a.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kumaliza mgogoro kati ya gereza na wananchi wa Kingale, tunapenda kupata askari ambao wataimarisha mahusiano na jamii inayolizunguka gereza tofauti na ilivyo sasa. Askari waliokaa muda mrefu gerezani pale wangehamishiwa maeneo mengine ili kupata askari wengine watakaoleta maarifa mapya ya maendeleo. Tunapenda kupata askari wenye taaluma ya mifugo, kilimo, umwagiliaji na wachumi ili kulisaidia gereza kujiimarisha kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Mji wa Kondoa umekuwa na unaendelea kukua, tunahitaji kupatiwa vifaa vya Jeshi la Zimamoto ikiwemo gari kwa maana hakuna huduma hiyo hali tukiwa tunashuhudia mali za wananchi zinateketea kwa moto na kusababisha hasara kubwa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi karibuni tumeshuhudia mabweni ya wanafunzi yakiteketea bila msaada wowote kwenye Shule ya Sekondari Kondoa Islamic na kituo cha kulelea mayatima cha Bicha, magari yameungua moto, viwanda vya mafuta ya alizeti vimeteketea na nyumba za wananchi. Tunaomba gari la zimamoto na vifaa vya askari wa zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu magari ya polisi yamechakaa sana tunaomba polisi wilaya wapatiwe gari la kufanyia doria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Wizara ya Afya. Nianze kwa kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayofanyika, lakini niwapongeze Wizara ya Afya kwa kazi kubwa wanayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo machache; jambo la kwanza, nimpongeze Dkt. Chandika ambaye ni Mkurugenzi wa Benjamini Mkapa, Hospitali yetu ambayo ipo hapa Mkoani, kwa kazi kubwa anazozifanya. Ombi langu kwa Wizara ni kwamba Hospitali yetu ya Benjamini Mkapa watu wote sisi Waheshimiwa Wabunge pamoja na wananchi kutoka maeneo mbalimbali tunakwenda kupata huduma ya afya pale, kwa hiyo wajitahidi kama Wizara kuhakikisha hospitali ya Benjamini Mkapa inatoa huduma kwa kiwango kama vile Muhimbili ama zaidi ya hapo. Wapatiwe vifaa vya kutosha na vyenye sifa na hadhi kwa sababu Benjamini Mkapa sasa Serikali ndio ipo hapa na mikoa mingi ya jirani tunategemea kwenda huko kwa sababu ni karibu kuliko Dar es Salaam. Kwa hiyo, tunaomba Serikali basi iiangalie hii hospitali kwa sababu sasa inatuhudumia wengi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naishukuru Serikali unakumbuka Bunge la Bajeti lililopita tuliongelea kesi za akinamama ambao walikuwa wanakufa kwa kukosa huduma za hospitali hasa kwenye Kata ya Suruke. Nilikwenda kwa Mheshimiwa Ummy Mwalimu ambaye alikuwa Waziri wa TAMISEMI kumweleza ile hali mbaya ya akinamama ambao walikuwa wanakosa huduma kwa sababu wako kisiwani.

Mheshimiwa Spika, leo hii ninapoongea Serikali imekwishajenga kituo cha afya kikubwa cha kisasa na tayari kinakwenda kukamilika. Ombi langu sasa kwa Serikali, katika nia ile ile njema ya kuwasaidia akinamama wale, sasa tunaomba katika mgao huu wa ajira basi tupatiwe madaktari japo watano ili waweze kwenda kukihudumia kituo hicho cha afya, wale akinamama ambao walikosa huduma nzuri ya uzazi wakawa wanapoteza maisha na watoto wao, basi waweze kupata huduma. Kwa sababu Serikali imekwishawekeza fedha nyingi na kituo kilikwishakamilika, ni vema sasa basi Waziri, Mheshimiwa Ummy atupelekee Madaktari ili msimu huu wa mvua unapoanza wale akinamama ambao wanajifungua kipindi hicho wasipate tena shida ya kuzuiwa na mto, ukizingatia daraja la mto bubu linapelekwa litajengwa mwakani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, tuna kituo cha afya kilijengwa Awamu ya Tano. Kituo kile cha afya kinaitwa kituo cha afya lakini hakijakamilika majengo, tunahitaji kupata jengo la OPD, chumba cha x-ray, pamoja na wodi ya akinamama na akinababa. Kwa hiyo ili kikamilike kile kituo cha afya na kiwe na sifa ya kituo cha afya, basi tunaomba yale majengo yakamilike.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri au bahati mbaya katika bajeti hii sikuona kama nimepata kituo cha afya, lakini sasa kama watatusaidia tukakikamilisha kile kituo cha afya ambacho kilijengwa Awamu ya Tano nab ado hakijakamilika, watakuwa wamefanya jambo jema sana.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, tuna vituo vya afya, tuna hospitali zetu, tunamwomba Mheshimiwa Ummy hospitali hizi ziweze kupatiwa vifaa pamoja na watumishi ili wananchi waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, nashukuru sana kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia nafasi, lakini na niungane kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maajabu anayotuonesha sisi Wabunge wa Majimbo katika kazi za maendeleo zinazofanyika. Baada ya kuyasema hayo niwapongeze Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa,

Mheshimiwa Rais hajawahi kukosea kwenye Wizara hii ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa. Tulianza na ndugu yetu Mheshimiwa Bashungwa, tunamshukuru tulienda vizuri na sasa tupo na dada yetu tunaamini kwamba, Mwendo uleule ataondokanao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuonesha kwamba, Wizara hii inafanya vizuri wanajiamini sana, hapa nimeshika document za kuonesha ni namna gani wametupelekea fedha kwenye majimbo yetu. Ninawapongeza nasema sawasawa, mko vuzuri, kule kujiamini kwenu kunasababisha na sisi kuwaamini ipasavyo, tunawaamini sana. Pamoja na mazuri na makubwa mliyoyasema, changamoto huwa hazipungui. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe sasa Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alisikilize hili ninalomwambia na amwambie Katibu Mkuu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ambaye naye pia tunamuanini sana, amuandikie mkurugenzi wetu wa Halmashauri ya Mji Kondoa, kufanya mabadiliko kidogo kwenye fedha hizi za boost kwa maana ya kwamba, tuna fedha ya kujenga madarasa shule ya msingi Mongoroma, shule hii ya Mongoroma imezidiwa sana, ina wanafunzi 987. Katika wanafunzi hao wanafunzi wanaotoka mtaa huo ni wanafunzi 502, wanafunzi 485 wanatoka mtaa mwingine na wanafunzi 29 kutoka kwenye mtaa huo tunaotaka tujenge hiyo shule wanatembea kilometa 6.5 na hawa wanaokwenda Mongoroma kutoka Selia wanatembea kilometa 4.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale tuliona sisi wananchi wa Selia tuanze ujenzi wa shule ya msingi, tunasema shule shikizi, na tumeanza kujenga madarasa mawili na matundu ya vyoo vinne, ili kunusuru hawa watoto wanaotembea kilometa 6 kwenda kusoma shule ya msingi mtaa mwingine. Kwa sababu, naamini ni makusudio ya Serikali kila mtaa uwe na shule ya msingi ili kupunguza umbali, basi nimuombe aruhusu haya madarasa sita ambayo yanakwenda Mongoroma yakajengwe pale Selia madarasa sita na yale ya kwetu wananchi, yatakuwa madarasa nane na vyoo vyetu vinne tukichukua na hivi vyoo tutakuwa tueweza kuwasaidia hawa watoto wetu na tutakuwa tumefanya jambo lenye tija sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Mongoroma kuna madarasa kumi ya shule ya msingi ambayo yote yanatumika. Kwa hiyo, tukiwabakiza wakibaki 500 hawa 400 wengine tukawatoa, watakuwa na sehemu ya kubaki na madarsa yao yanayowatosha wao na wale wa mtaa mwingine tutakuwa tumewasaidia kupunguza umbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nimuombe Mheshimiwa Waziri. Tumekwisha kamilisha shule kama mbili shikizi, zina sifa ya kusajiliwa, lakini tumekuwa wazito sana kwenye kuzisajili hizi shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri hebu wape maelekezo tuzisajili, mbona tumejenga shule ya sekondari hii mpya, tumeisajili mapema na leo tuna kidato cha pili kwenye sekondari yenu ambayo tunawashukuru sana, mmetusaidia sana watu wa Kondoa kupunguza idadi ya wanafunzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajira kwa walimu pamoja na huduma ya afya, Wizara ya Afya, wauguzi, tuna tatizo kubwa kwenye shule zetu. Ukienda shule moja ya msingi Hachwi unakuta ina mwalimu mmoja na ni shule kongwe. Tunaomba msaidie, specifically, tupeleke walimu Shule ya Msingi Hachwi. Na ikiwezekana hizi ajira mpya tuchague sisi wenyewe, yaani sisi tuwapeleke walimu moja kwa moja kwenye shule na ikiwezekana tuwaambie tunatangaza ajira Shule ya Msingi Hachwi, tunatangaza ajira Shule ya Msingi Serengeni, tunatangaza shule ya msingi hii kwa hiyo, anayeomba ajue kabisa anaomba kupelekwa shule ya msingi fulani na kama hataki akatae moja kwa moja atafutwe ambaye atakubali kwenda as long sasa hivi mmefanya kazi nzuri za miundombinu. Kondoa inafikika sehemu zote hakuna haja ya mwalimu kushindwa kwenda kufundisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine kutokana na muda, niwapongeze kwa TARURA. Kwa kweli, mnafanya kazi vizuri sana, huyu Engineer Seif huyu anapaswa apewe hiyo haki yake kwa sababu, hatumsumbui sana isipokuwa kazi zake tunaziona, anapiga kazi sana. Kwa hiyo, tumshukuru, lakinis sasa pale kwetu kuna barabara moja muhimu sana ambayo ni ya kwake, inatoka Iboni kwenda Bilisa, ni barabara changamoto sana. Wananchi sasa wanatembea kwa miguu karibu kilometa saba kuja kutafuta mahitaji mjini, hapo mwanzo kulikuwa na gari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna madaraja mawili-matatu pale ya kwenda kuyajenga. Hebu tusaidieni tuyajenge madaraja yale mtakuwa mmetusaidia kwa sababu, kwanza barabara yenyewe kwa umuhimu wake ndio barabara pekee ambayo inaweza ikawa mbadala wa barabara ya kwenda mikoa yote, kuunganisha Mkoa wa Dodoma na Manyara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kwa harakaharaka kutokana na muda, kuna haya mapato ya halmashauri. Sisi tuko Halmashauri ya Mji, Mheshimiwa Waziri usitufundishe uwoga wa kutafuta mapato, tunaomba uruhusu ile asilimia 40 ile ya maendeleo tuendelee kupambananayo kwa sababu, inatusaidia sana na hakuna mahali tunaweza kusema tumefeli, lakini leo kutupunguzia kutupelekea asilimia 20 maana yake hata mikopo ya wale vijana wanawake pamoja na mikopo ya wenye ulemavu itapungua sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaendelea kuwakopesha milioni tatu, milioni nne, sasa ukipunguza zaidi tutakuja kuwakopesha kiwango kidogo kutokana na hiyo asilimia 20. Tuna uwezo wa kuendelea kujibana tuisaidie Serikali Kuu kufanya miundombinu ambayo tuna uwezonayo, leo tumeweza kujenga angalao zahanati mbili kwa kipindi cha mwaka huu mmoja. Sasa ukipunguza hicho kiwango cha fedha tukawaachia tu watendaji wakaendelea kuzitumia hata Madiwani watakata tamaa katika kusimamia mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri turudishieni asilimia 40 ya maendeleo ili wale wananchi tunaokwenda kuchukua kodi zao kule waweze kuona matunda ya fedha wanazolipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi huu wa tactic, watu wa Kondoa tunasubiri sana barabara za lami na Taa, tunasubiri sana. Sasa tunaomba utusaidie kwa sababu ni mji, tujenge barabara zetu kwa lami kama jinsi mpango wa Serikali ulivyo kwa hiyo, tufupishie ule urefu wa mradi huu ili tuweze kuupata kwa pamoja na tukienda 2025 tuwe tayari tumekwishaweza kuweka lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia. Mheshimiwa Waziri nikuombe, kabla bajeti hii haijaisha tuwe tayari tumeanza ujenzi wa sekondari mpya ya Bolisa kwa sababu, tuliomba sekondari mbili, moja ile mmetupa tumekamilisha, lakini sasa hii ya Bolisa tunaomba na yenyewe ianze kujengwa kabla ya bajeti hii kuisha. Hilo ukilifanya utakuwa umetutendea haki sana wana-Kondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, ikumbukwe kwenye hizi sekondari mpya ambazo tumezijenga, ilikuwa ije shilingi milioni 600 mpaka leo zimekuja milioni 470. Tumekamilisha na watoto wanasoma, lakini bado katika yale ambayo tulikuabaliana kwamba, shule hizi zinatakiwa ziwe pia na nyumba za walimu. Kulikuwa na milioni 130 hatujajua zimekwamia wapi mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Mheshimiwa Waziri, Serikali ifanye kila la kufanya shule zilizojengwa ni mnzuri sana zitakuwa na fursa zaidi endapo walimu wetu hawatatembea mbali. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri zile milioni 130 ili tumalizie miundombinu, nyumba za walimu, pamoja na mfumo wa maji ambao unasoma katika shule ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nikushukuru sana na niendelee kuipongeza Serikali. Shukrani. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Ally Makoa.

MHE. ALLY JUMA MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu lakini pia nimshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyowatendea wananchi wa Jimbo la Kondoa, especially kwenye hii sekta ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Kaka yangu Mheshimiwa Aweso Waziri wa Maji, Naibu Waziri, nawashukuru wizara kwa ujumla Katibu Mkuu na watendaji kwa sababu wote hawa ni watu wema sana na ni msaada mkubwa sana katika muda ule ambao tunahitaji huduma kwa ajili ya wananchi wetu. Mungu awabariki awape nguvu waendelee kuchapa kazi na waendelee kuiheshimisha nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaishukuru Serikali kwanza kwa kukubali maombi yetu wana kondoa mjini kuweza kutenga fedha kwa ajili ya miradi yetu ambayo inaendelea. Mradi wa Hachwi, Murua na Mradi wa Bicha pamoja na Mradi mkubwa wa Kondoa Mjini. Pia naishukuru Serikali kwa kuweza kutukamilishia uchimbaji wa visima nane kwenye mitaa nane ambayo kwa kweli natoa pongezi nyingi sana kwa miradi hii na kwa kweli imekamilika, ispokuwa kisima kimoja na ambapo si tatizo la wizara ni tatizo la kule kwetu nadhani tutalifanya vizuri, mkandarasi alipata changamoto kidogo Kisima cha Itiso. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niishukuru Serikali yangu kwa kukubali maombi yetu wana kondoa Mjini, kupanua mradi wetu wa maji Kondoa Mjini kwa ajili ya Mitaa yetu ya Kwapakacha, Mtaa wa Bicha, Tura pamoja na Mitaa ya kichangani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru sana Serikali kwa kukubali kutenga fedha kwa ajili ya kutuchimibia visima kwenye maeneo matatu, mitaa ambayo kwa kweli ilikuwa haina mradi wa maji ambao ni Mtaa wa Chang’ombe ambao uko Kondoa Mjini maarufu Serengenyi, lakini Mulua pamoja na Mtaa wa Damai. Ninaishukuru na kuipongeza Serikali kwa kutukubalia maombi yetu sasa wametenga fedha kwa ajili ya kwenda kutoa huduma hiyo kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani ni nyingi kwa sababu miradi ni mikubwa sana. Hapa sasa baada ya kuipongeza Serikali ninaushauri wa mambo kama matatu ambayo kwa kweli yakifanyiwa kazi haya yataleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri namba moja; tumekuwa tukichimba hivi visima kama alivyotangulia kusema mwenzangu halafu vinachukua muda mrefu sana. Kwa sababu tunachimba kisima mwaka huu, mwaka ujao tunafanya designing lakini mwaka mwingine pengine ndio tunaweza kuanza kuwasambazia wanachi. tumechimba vizima vinane ambavyo kwa kweli wananchi wamepata matumaini kubwa sana lakini mpaka leo hatujaanza kuvisambazia. Visima hivi vipo Chora, Ausia, kwamtwara, Tamkori, Chemchem, Hurumbi, Dumi pamoja na Seria, Munguli na Msoi. Nimeona hapa kuna baadhi ya visima ambavyo tayari vimetengewa fedha kwa ajili ya usambazaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilikuwa nashauri hapa Serikali, kwa sababu wananchi wana kiu ya maji na wananchi wanapata shida na wanakwenda mbali, Serikali inapopanga kwenda kuchimba visima basi japo wakati tunasubiria kufanya usambazaji mkubwa ule wa fedha, fedha nyingi kwa ajili ya usambazaji, basi watuwekee japo sehemu moja kwa ajili ya wanachi kuchota maji wakati tukisubiria kuja kusambaziwa, lakini na sehemu moja kwa ajili wananchi kuweza kunywesha mifugo yao. Itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuwe na miradi ambayo tunafanya designing and building kwa wakati mmoja japo tuwe na eneo dogo la wananchi kupata maji. Natolea mfano, kuna huu Mtaa wa Chora, huu wanapakana na hifadhi, wanapokosa maji hasa kipindi cha kiangazi inawalazimu kuingiza ng’ombe kwenye hifadhi. Sasa tunaleta mgogoro kati ya wananchi na hifadhi na wananchi wetu wanaonewa kwa kupigwa faini kubwa hali ya kuwa wanatafuta maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hawa watu wa Hurumbi, wanapakana na Pori hili la Swagaswaga. Kipindi cha kiangazi wanapata sana shida ya maji matokeo yake wanaingiza ng’ombe kwenye hifadhi. Hata hivyo, ni hekima za watu wa pale Swagaswaga wanawaruhusu wakati mwingine kwenda kunywesha kwenye hifadhi lakini hii pia ni mgogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili kuwasaidia watu hawa inabidi basi kisima tumechima basi watolewe maji japo wapewe DP moja pamoja na eneo la kunywesha mifugo litakuwa linawasaisia, huo ni ushauri wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wa pili; tuna mfuko wa maji ambao unafanya vizuri. Nikushukuru Mheshimiwa Waziri, juzi wakati tunafuatilia fedha kwa ajili ya mkandarasi wetu wa Kondoa Mjini, tulizungumza mambo mengi na tulikubaliana na nimeona matumaini ndani ya wiki hii. Mungu awabariki sana, maana yake mkandarasio wetu atapata fedha zake na ataendelea na mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna mfuko huu wa maji, ambao kwa kweli kwa nini mfuko huu usingekuwa unapeleka fedha kwa wasimamizi wa huduma moja kwa moja kama wanavyofanya watu wa barabara? Ili kuepuka kuchelewa kuwalipa wakandarasi ambapo sasa hivi mpaka wa-arise certificate itembee kwenye ofisi nyingi inachukua muda mrefu wakandarasi wasio na uwezo wanashindwa kumalizia miradi. Tukifanya kama wanavyofanya watu wa barabara, fedha hizi za mfuko wa maji zikaenda kwa wale wasimamizi wa huduma mikoani au wilayani inaweza ikasababisha wakandarasi wakawa wanalipwa kwa wakati na miradi ikakamilika kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu; ambalo nataka nitoe ushauri kwa Serikali. Kuna changamoto kwenye vile vyombo vya watumiaji wa huduma za maji wanaita CBWCO. Unakuta vyombo hivi vinatumia gharama kubwa kuliko makusanyo ambayo yanafanywa na watumiaji wa maji vijijini. Kwa sababu wachangiaji wa vijiji vingi sio wengi sana kitendo ambacho kinafanya mapato yanakuwa madogo matumizi yanakuwa makubwa, tunawalipa mafundi na wanalipa pia wahasibu. Kwa nini Serikali isingeajiri watu hawa ili kupunguza burden (mzigo) kwa wananchi ambapo kweli maeneo mengi ambayo wanatumia hiki chombo cha maji wanalipwa, wamekuwa wakishindwa kuendesha miradi kwa sababu makusanyo ni kidogo matumizi ni makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ninaombi ambalo Mheshimiwa Waziri, unapaswa ulichukue na ulifanyie kazi. Tunafanya Mradi mkubwa pale Kondoa Mjini na tumeuongezea ukubwa wa takribani bilioni Nne. Kwa sababu Mkandarasi wetu yule ambae tunashukuru mlitupatia mkandarasi mzuri pamoja na changamoto lakini mpaka sasa ameweza kufikia zaidi ya asilimia 72. Sasa kwa sbabu ukame na hali mbaya ya maji ilikuwa kwenye Jimbo la kondoa Mjini… ilifikia Waziri Mkuu alikuja…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ally Makoa, ahsante sana.

MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa tu na ombi dogo kwamba Mradi huu ukikamilika basi Mheshimiwa Aweso, amlete Waziri Mkuu, auzindue ule Mradi kwa sababu wananchi walipata shida na sasa wana neema kubwa. Ni hilo tu na baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi. Awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna alilvyoonesha mafanikio makubwa sana kwenye Wizara mbalimbali hususan hii Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa miradi mikubwa ya reli, barabara, bandari, ununuzi wa ndege na miradi mingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nitoe shukrani zangu kwa Wizara inayoongozwa na Mheshimiwa Mbarawa pamoja na Naibu Mawaziri wawili, Katibu Mkuu na Watendaji wote niwapongeze kwa juhudi kubwa za kumsaidia Mheshimiwa Rais katika kutekeleza majukumu haya ya kuitengeneza Tanzania katika ubora wa viwango. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo machache, kwanza nishukuru Wizara kupitia Mheshimiwa Mbarawa kwa kukubali kuingiza ile Barabara ya kutoka Dalai – Mondo kwenda Bicha ambayo ndiyo iliyokuwa imetajwa kwenye Ilani na baadaye kidogo kukawa na sintofahamu, lakini baada ya kutusikiliza ameamua kuirudisha, namshukuru sana, hii kilometa 35, sasa ni habari njema kwa Wakazi wa Kondoa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nishukuru pia Serikali kwa kukubali baada ya miaka miwili sasa imekubali kutupelekea fedha kwa ajili ya kipande kidogo kile cha kilometa 0.8 kutoka NMB mpaka National Milling. Nimeona kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri kwamba kipande hicho wamekiingiza, nawashukuru sana Wizara ya Ujenzi kwa kutupa faraja na matumaini. Ikumbukwe kwamba hii ni bajeti ya tatu, bajeti zote mbili hatukupata bahati ya kutengewa fedha na ndiyo kipindi hiki tumetengewa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa nina concern ndogo kwamba barabara hii ipo kati kati ya mji, lakini inapoanzia pale Magereza mita 100 kuna mto mkubwa ambao masika yote huwa hapapitiki. Nawakumbusha Wizara pale kunatakiwa lijengwe daraja. Kwa hiyo wafahamu hilo kwamba barabara yao hii inayoingia mjini katikati kuna daraja ambalo linatakiwa lijengwe la TANROADS. Daraja lililopo ni dogo sana ambalo linamilikiwa na TARURA na limekuwa likileta athari kubwa kwa wananchi na limekuwa likisababisha ajali kutokana na udogo na daraja lenyewe ni la muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, wiki mbili zilizopita niliuliza swali juu ya barabara hii na majibu ya Serikali yalikuja kwamba tutatengewa kilometa tatu za lami mjini ikiwepo kipande hiki cha kilometa 0.8, lakini kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri sijaona kama hizo kilometa tatu zimeinishwa pale. Kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Waziri kama kulikuwa na kausahaulifu kidogo nikumbushe tu, majibu ya Serikali wiki mbili zilizopita tuliambiwa tutapewa kilometa tatu ambayo kilometa hizi 2.2 ambazo zitakuwa zinatokea TANESCO kuelekea Daraja la Munguri B. Kwa hiyo niombe waingize hiyo kwenye bajeti ili iwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, leo hoja kubwa iliyopo katika Jimbo la Kondoa Mjini ni lile Daraja la Munguri B. Tunaishukuru Serikali ilitutengea shilingi milioni 600 katika bajeti hii tuliyonayo na katika bajeti hii tumeona kuna shilingi milioni 150. Tunaishukuru sana Serikali, lakini Mheshimiwa Mbarawa akumbuke, aliposimama Mheshimiwa Rais pale Bicha, hoja aliyomuuliza ni juu ya daraja hili na akalitolea maelezo. Kwa kweli ujenzi wa daraja hili ni muhimu sana kutokana na uchumi wetu ambao watu wengi wanalima eneo la pili la Mto Bubu, lakini pia tumefungua utalii kwenye Pori letu la Swagaswaga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunaomba daraja hili walitilie mkazo at least ukifika mwezi wa sita itangazwe tender kama zilivyotangazwa za madaraja mengine ya Mkoa wa Dodoma. Kwa hiyo hili naomba Waziri alichukulie maanani kwa sababu hakuna hoja kubwa zaidi ambayo Mheshimiwa Rais anaweza akauliza sasa hivi katika Jimbo la Kondoa Mjini zaidi ya daraja hili.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, TANROADS walipita Barabara ya kutoka Dodoma kwenda Babati ilipita ikamega eneo la Shule ya Msingi Nkuku na kukawa na mazungumzo ya kulipa fidia ili ile shule tuiondoe pale tuipeleke sehemu nyingine. Niombe Wizara kwenye bajeti hii watutengee fedha ili tuiondoe ile Shule ya Nkuku tujenge shule nyingine ya msingi kwa ajili ya kunusuru madhara ambayo yanaweza yakajitokeza kwa sababu ile shule sasa hivi iko barabarani sana. Kwa kweli Wizara ya TAMISEMI wametuletea shilingi milioni 370 za ujenzi wa shule ya msingi mpya. Kwa hiyo nadhani ni kiwango hicho hicho ambacho TANROADS wanapaswa watutengee kwa ajili ya kunusuru maisha ya watoto ambapo shule ile iko barabarani.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ili kuchangia Wizara hii ya Ardhi. Awali ya yote nimshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake nzuri juu ya Wizara hii. Kwanza kwa kuona umuhimu wa Wizara hii, Mheshimiwa Rais ameridhia kuunda Kamati kwa ajili ya kushughulika migogoro ya ardhi. Hili ni jambo kubwa ambalo kwa kweli likikamilika litaleta tija kwenye nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, utaona amefanya mabadiliko kwenye Wizara hivi karibuni na ametuletea Naibu Waziri huyo hapo, tunamwona lakini na Katibu Mkuu mpya. Yote hii ni kutaka kuendelea kuimarisha hii Wizara, lakini Mheshimiwa Waziri yuko pale dada yetu Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula anaimudu hii kazi na ndio maana Mheshimiwa Rais kaendelea kumwamini. Kwa maana hiyo tunajua kwa safu hii iliyopangwa sasa hivi, tunawapa muda ili kuweza kushughulikia haya majadiliano na michango ya Waheshimiwa Wabunge kuhakikisha angalau tunakwenda kupunguza hii migogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru, leo utaona asilimia kubwa ya Waheshimiwa Wabunge wanachangia kuhusiana na migogoro, itafikia mpaka kipindi tutashindwa kuona kazi nyingine ambazo zinafanywa kwenye Wizara hii. Mheshimiwa Rais amemtoa Engineer Sanga kule Wizara ya Maji akamleta huku na sisi tulikuwa na mawazo kwamba tunataka sasa Wizara ya Ardhi tuanze kulipa kodi ya ardhi kupitia simu. Tunawapongeza Wizara sasa hivi tunaona tukiwa majumbani tunapata meseji na zenye control number na tunaanza kulipa kwa urahisi. Kwa maana hiyo tunaona mwendelezo mzuri na tunawatia moyo waendelee kushughulika na jambo hili ili na hii Wizara ionyeshe mchango wake mkubwa kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia huu mkopo umekuwa ukizungumzwa hapa na Wabunge, of course mkopo una mambo mengi mazuri ambayo tukiyafanya italeta tija kwenye Taifa, michango ya Waheshimiwa Wabunge ni kuhusiana na matumizi hasa ya fedha hizo, lakini tunaamini viko vitu. Wakinunua mashine, mitambo wakatujengea ofisi hizo na vitu kama hivyo, vitaleta tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wengi wanaona ni nanma gani kunakuwa na migogoro mingi na ndio maana wote tunatamani ardhi yetu yote ingepangiwa matumizi bora ya ardhi ili kuondoa migogoro. Sasa hapa Mheshimiwa Waziri aendelee kuchukua ushauri wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii na aendelee kuufanyia kazi. Nakumbuka mwanzo walikuja na vijiji 250, baada ya ushauri wa Kamati, leo wamekuja na vijiji 500, bado Kamati inaona ipo room ya kuendelea kuongeza idadi ya kuvipima vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo hotuba ya Kamati ni nzuri na waendelee kuichukua kama Wizara na waendelee kuifanyia kazi. Waone namna bora ya kuweza kuongeza idadi ya vijiji. Katika ule mkopo nilikuwa naona fedha zile zilipangiwa Kamati nyingine tofauti ya kuendelea kushughulika na zile fedha. Nadhani tunaongelea Tume ya Mipango ya Ardhi kwa sababu tunaamini wale ukiwapa fedha leo, leo hii wanaingia site kwa haraka na kwa kutumia vifaa vyao hivyo hivyo wataendelea kuvipima vile vijiji hata kama hiyo Kamati nyingine itakuwa haipo. Kwa hiyo, waendelee kuuchukua ushauri wa Kamati, ushauri wa Wabunge, waone namna gani wanaweza kuboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi jimboni kwangu; tuna migogoro ya ardhi kama ilivyo katika majimbo mengine, lakini sasa kwangu kuna migogoro miwili, mgogoro kati ya wananchi wa Mongoroma na Pori la Swagaswaga ambalo Mheshimiwa Rais alilitolea maelekezo. Sasa Mheshimiwa Rais anatoa maelekezo, lakini kule kazi nyingine zinaendelea za kuweka vigingi. Sasa kabla Wizara ya Ardhi haijakwenda kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais, kazi nyingine zinaendelea. Hapa inaonekana sisi kama Wizara ya Ardhi tunakuwa nyuma, tunachelewa kwenda kufanya maamuzi ambayo yangesaidia kuondoa hii migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo wito wangu bado Mheshimiwa Waziri kuna maelekezo ya Mheshimiwa Rais kwamba kufika kule ambapo Kamati ambayo yeye ndiye Mwenyekiti walielekezwa kufika, hawakufika kama Kamati, lakini hali iliyopo kule kwa kweli sio nzuri, wananchi wanashindwa kuendeleza maeneo yao. Kwa hiyo, ni lazima kwenda kuutatua ule mgogoro ili kuwaweka wananchi wetu vizuri, waweze kufanya kazi zao za maendeleo wakiwa na amani kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la King’ang’a na Wananchi wa Kingale, jambo hili wamelishughulikia vizuri, tunawashukuru sana na mgogoro ule umekwisha. Wizara ilikwenda, Waziri alimtuma Mpimaji na ramani Mkurugenzi, amefika kule kafanya kazi yake vizuri. Kachukua mapendekezo yamefika mpaka kwa Mheshimiwa Rais, kwa ukarimu wa Mheshimiwa Rais ameridhia yale mapendekezo na ni mapendekezo ya wananchi. Cha ajabu juzi anakwenda Mkuu wa Gereza anakamata ng’ombe wa wananchi anawapiga faini. Najiuliza hivi kila idara, kila mtu anaamua tu kukamata ng’ombe wa watu na kuwatoza faini, hawa wananchi fedha hizo wanatoa wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Bwana anaitwa Juma Kanene ametozwa faini ya 150,000; kuna Bwana anaitwa Hamis Mwiguu ametozwa 400,000; na kuna Bwana anaitwa Kiteto Kiteto ametozwa 200,000; Bwana John ng’ombe wake wawili wamezuiliwa gerezani na huyu Bwana Samweli ng’ombe amezuiliwa gerezani. Sasa tunajiuliza kila mmoja akijipa jukumu la kukamata ng’ombe wa wananchi na hali ya kuwa eneo hilo tayari limeshakwishatatuliwa mgogoro wake, imebaki Wizara ya Ardhi kwenda kutuonesha tu mipaka tuliokubaliana, hii inakuwa sio sawa na inakuwa ni uonevu kwa wananchi. Kwa hiyo, naomba mamlaka iliyopo hapa ikiwemo Waziri wa Mambo ya Ndani amwelekeze Mkuu wa Gereza awarudishie wananchi fedha alizochukua kwa sababu si halali yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara sasa iende ikakamilishe jambo hili, lililobaki ni kuwaonyesha tu wananchi kwamba Mheshimiwa Rais katupa maelekezo kwamba ninyi mpaka wenu unaishia hapa na gereza unaishia hapa. Tuwasaidie kuweka vigingi ili kila mmoja aweze kujua mpaka wake ili wananchi wetu hawa waweze kufanya kazi zao kwa amani bila kutishiwatishiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikipata nafasi ya kuja kuchangia kwenye Wizara ya Mambo ya Ndani nitashauri juu ya uendeshaji wa lile gereza kwa sababu tunaona halina tija kwa safari hii, inabidi tulifanyie mapinduzi ili liweze kuleta tija katika nchi na wananchi wa eneo lile waweze kunufaika na gereza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Na mimi nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzani Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa anavyoendelea kuilea hii Wizara akiwa na matumaini makubwa kwamba ni Wizara ambayo kiukweli ikitendewa haki yake kutokana na wingi wa vivutio tulivyonavyo itaweka mchango mkubwa sana kwenye Pato la Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuona hayo ameendelea kufanya mabadiliko. Utaona amembadilisha Mheshimiwa Mchengerwa na Katibu Mkuu wake wote wameletwa kwenye Wizara hii. Lengo ni kuchochea ufanisi katika Wizara ili Taifa liweze kupata mapato kutokana na hifadhi zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampongeza Mheshimiwa Waziri Mchengerwa kwa namna alivyoanza kuyatekeleza majukumu yake kwenye Wizara hii, na ninaamini ataiweza. Ni Wizara ngumu lakini ninamfahamu kidogo, nimeweza kukaa nae nikiwa bosi wake kule Pwani, nilikuwa nikimfutilia, naamini ataiweza kazi hii. Kama alivyoweza Wizara ya Michezo sina mashaka naye. Lakini pia ana Naibu Waziri mzuri. Akiweza kumtumia vizuri Naibu Waziri wake ni mwanamke jasiri pia, ni jasiri na utaona hata kwenye matamko yake na yuko serious na kazi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yake ina changamoto kubwa mbili. Changamoto ya kwanza ni migogoro baini ya hifadhi zake pamoja na vijiji, na changamoto ya pili ni mwingiliano wa wanyama na binadamu. Hizi ni changamoto kubwa ambazo atategemea either zitamsumbua ama Mungu akimjalia akizipatia basi atakuwa ameweza kuitendea haki Wizara hii. Ataweka historia kubwa katika nchi hii, na unaona hata mwelekeo wa bajeti tunavyochangia hakuna ukali sana, kwa sababu tuna matumaini makubwa kwamba amekuja hapo pamoja na Katibu Mkuu wakishirikiana vizuri na Makamishna wale, ni watu wazuri. Wana Bodi nzuri, na kwa kweli wakishirikiana wataitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la mifumo ya makusanyo tunaona wanaenda vizuri na tunaona ongezeko la watalii pamoja na fedha katika Taifa letu. Sasa waendelee kuimarisha hivyo ili wampe moyo Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la migogoro ya mipaka mimi nishauri jambo moja. Mheshimiwa Waziri hebu usirithi hii migogoro kwa maana ya historia yake, hebu jaribu make sasa vizuri wewe na cabinet yako yote muanze kuiangalia hii migogoro. Kuna migogoro mingine inaweza ikatatuliwa kwenye ngazi ya mapori yenyewe. Kuna baadhi ya maeneo, mimi nilipata bahati mmeniletea pale swagaswaga kijana Reuben ni kijana mzuri sana kwenye pori la swagaswaga, ni mkuu wa pori lile. Yeye ametumia mfumo wa kushirikisha wananchi katika ku-solve migogoro iliyopo katika eneo lake, na amefanikiwa sana. Ni kwa mara ya kwanza Reuben amekuwa akisifiwa na wananchi wa Kondoa wanaozunguka lile pori kwa sababu kwanza anafikika na anawafikia watu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi wameweza kutatua mgogoro wa mpaka ambao ulikuwa unataka uzuke kwenye maeneo ya Iyoli, Kingale na Tampori. Wamekuja maafisa ardhi walikotoka hatujajua wametoka wapi? wakaweka mipaka mipya iliyoanza kusababisha taharuki kwa wananchi. Wananchi waliponipigia nikampigia mkuu wa pori Bwana Reuben, amekwenda kwa wananchi wakashirikiana kwenda kuitambua mipaka ya asili na wakaiyona. Jana walikuwa wanashirikiana kuhamisha vile vigingi ambavyo viliwekwa kimakosa kuvirudishia pale, na hivyo mgogoro ule automatically unaondoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo nikushauri kwamba hata ile taarifa ya Mawaziri nane usiitegemee sana, sehemu kubwa itakupotosha tu, kwa sababu kiukweli haijafanya kazi kama alivyokusudia Mheshimiwa Rais. Tumia sasa nafasi uliyonayo na nafasi yako wewe kwenda kuijua hii migogoro, utaimaliza kiuraisi kama ulivyoweza kwenda Mara kule kwa watani wetu hawa wakakuelewa, ukija pale Kondoa kwa Warangi watakuelewa tu. Kwa sababu ni watu waele sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgogoro ambao uko pale Mongoroma ambao unasababisha wananchi wanashindwa kufanya kazi zao. Tunauita mgogoro ni kwa sababu tu tunaendelea kukubali kurithi maneno ya migogoro. Lakini hata ukimwagiza Reuben akaenda akaonyeshwa mipaka ambayo wananchi walishirikiana na wale waliyotangulia ataiona na atatoa hivyo vigingi vipya vilivyowekwa atavihamisha wananchi wataendelea na maisha yao. Kuna maeneo kama hilo nalozungumzia kuna wakazi zaidi ya 4,000 wakazi zaidi ya 2,000 wamekaa muda wote wanawajukuu na vitukuu leo kuu-solve mgogoro ule huwezi ukasema uwaondoe wale watu ilhali huna pakuwapeleka. Lakini kama tutafuata maelekezo ya Mheshimiwa Rais ambayo alielekeza ile kamati kwamba kama maeneo yenyewe si mazalia ya wanyama na kama maeneo yenyewe si chanzo cha maji na wananchi wameisha kaa muda mrefu kuna haja gani ya kusema kwenda kuwatoa na hauna pakuwapeleka pale? nikuwaacha waendelee kukaa, kateni lile eneo waonyesheni wananchi mipaka yao ili waendelee kuishi na kujenga nyumba nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wanashindwa hata kujenga nyumba kwa sababu ya hizo taharuki ambazo zisizo na msingi. Kwa hiyo ninakushauri Mheshimiwa Waziri, ni vema sasa wewe mwenyewe ukimtumia Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watalamu ulionao kwakweli mnaweza mkafanya mambo makubwa na mkaacha hizi hifadhi zikabaki kuwa salama. Hakuna namna leo mtawaweka salama hata askari wetu, kwa sababu leo kama kutakuwa na migogoro kati ya askari wetu wanaolinda kule na wananchi hatutafanikiwa kutunza hifadhi zetu vizuri. Lakini kama wananchi hawa watakuwa sehemu kama wale niliokwambia, wananchi wa Iyoli na Tampori ambao baada ya kuu-solve huo mgogoro sasa wenyewe wamekuwa ni walinzi. Ibaki sasa wananchi wawaombe tu kwamba tunaombeni mtuongezee maeneo halafu iwe ni hiari kwenu kuwapa au kutowapa lakini wawe wanajua haya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo naweza nikakushauri sasa, ameongea vizuri Mheshimiwa Mbunge wa Malinyi, aliongea vizuri kuhusiana na mfumo za ajira za askari wetu hawa. Pamoja na ule mchango wake mzuri aliyoutoa nikuombe Mheshimiwa Waziri uangalie askari wetu hawa wote, wote askari hawa ni askari wa hifadhi wanasoma chuo kimoja, wanalinda wote tembo, wanalinda simba na mahifadhi yote wanalinda wao. Isije ikatokea sasa kuna taasisi nyingine wanapewa mishahara mikubwa na taasisi nyingine wanapewa mishahara midogo matokeo yake ufanisi unakuwa hakuna. Ndiyo maana unapata vijana ambao wanakwenda swaga ng’ombe za wananchi kwenye hifadhi halafu wanazichukua wanakwenda kuwapiga faini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu wanakuwa hawana, kipato chao kinakuwa kidogo; na kama ilivyo kawaida, kwamba wanadamu huwa tuna wivu. Kwamba kwanini wenzetu walipwe kikubwa sisi tulipwe kidogo. hebu fanyeni ku-harmonize watu wote/askari wetu wote walipwe sawa. Makamishna wote wawe sawa katika level hiyo hiyo wote wafanane ili kuwe na ufanisi mzuri na isipatikane askari anaetamani kwenda kwenye taasisi nyinge kutokana na malipo madogo yanayopatikana kwenye taasisi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo ninakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipatia nafasi na mimi niweze kuchangia mawazo yangu na wananchi wapiga kura wa Jimbo la Kondoa Mjini kama namna wanavyopenda itokee katika Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa neema na niishukuru Wizara kwa kazi kubwa ambayo inafanywa katika maeneo mbalimbali. Mimi ninaomba nichangie specifically kwenye Jimbo langu kwa sababu zipo changamoto ambazo zinawakumba wananchi wa Jimbo wangependa wapate majibu ya Serikali Wizara na mimi kama Mbunge wao nipate majibu hasa ya kuwajibu baada ya kuwa na changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja specifically nakwenda kwenye Kata inaitwa Bolisa kwanza ifahamike naongoza Jimbo la Mjini, Halmashauri ya Mji wa Kondoa kwa hiyo mimi nina mitaa sina vijiji. Ninayo Kata inaitwa Bolisa hii Kata ina mitaa mitatu ilipata mradi wa REA toka mwaka 2019, Mkandarasi aliyepewa kazi ile aliondoka mpaka wiki hii ndiyo niliambiwa amerudi lakini pamoja na kurudi kwenyewe bado kuna viporo ambavyo hakuvimaliza. Lakini ukiacha viporo ambavyo hakuvimaliza nimeambiwa kwamba scope yake imeisha lakini kuna mitaa miwili katika hiyo mitatu haikupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wananchi wa Kata ya Bolisa mara zote wanaipigia simu wakitaka kujua kwamba kwenye mradi wa REA ndiyo umeishia pale? Kwa sababu hata nilipohudhuria kwenye maonesho pale nilikutana na meneja wangu na watu ambao tumekuwa tukihangaika namna ya kuona tunaweza tukaukwamua ule mradi. Kwa hiyo, ningependa Mheshimiwa Waziri anisaidie kupata kujua ule mradi umeishia pale? Kama umeishia pale maana yake ni mtaa mmoja tu ambao ni nguzo zimefika pale, wananchi walishafanya wiring toka mwaka 2020 mpaka leo wanasubiria umeme, wana mashaka pia wanataka kujua mradi ule wa REA kama umeishia pale nyumba namba moja imewekewa umeme kwa Shilingi 27,000. Je, ile ya pili mradi ulipokomea wao watawekewa kwa 27,000 au watawekewa kwa hiyo 300,000?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nataka tupate kujua kwa sababu kuna changamoto kuna Kata inaitwa Suruke, Kata hii ina mitaa yake, Kata pamoja na mitaa hakuna nguzo hata moja iliyowahi kwenda. Kwa hiyo, ni Halmashauri ya Mji lakini Kata yote haina hata nguzo iliyosimama kwenye ardhi ya Kata ile. Katika kufuatilia sijaona hasa mpango hasa wa kuona kwamba Kata ile ni lini hasa itapelekewa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekutafuta Mheshimiwa Waziri sikupata bahati ya kukutana na wewe lakini nilikutana na Mheshimiwa Naibu Waziri, akawa amewasiliana na Mkurugenzi Ndugu yetu Seif lakini nawashukuru yeye Engineer Seif pamoja na Kasomambutu walifanya mawasiliano walikwenda kutembelea hiyo mitaa ninayoisema waliona hali halisi. Sasa nitaka kujua hii Kata hasa ya Suruke na yenyewe itapelekewa umeme kwa maana ya REA au tunategemea kuwapelekea kwa zaidi ya shilingi 300,000 au shilingi 600,000, shilingi 900,000 au shilingi 1,000,000? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni hili la utata wa bei ya kuwaunganishia wananchi umeme, ni kweli ile ni Halmashauri ya Mji ina mitaa badala ya vijiji lakini ndugu yangu kutoka katikati ya mji unakwenda hizo Kata ni kilometa nyingi na kazi pekee inayofanyika kwenye Kata zile ni kilimo na mifugo. Maana yake siyo tu vijiji vinavyokua bado ni vijiji mno, mwananchi anajenga nyumba yake kwa kipindi cha miaka mitatu au minne sana katumia gharama kubwa 200,000 leo ukimwambia mwananchi huyu ukamuunganishie umeme kwa shilingi 300,000 bila nguzo akiongeza mita 60 shilingi 600,000 yule mwananchi hana uwezo wa kulipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia hata watumishi tu Walimu hivi kweli mtu anaweza kuunganisha umeme kwa hali ilivyo katika vijiji vyetu, hii mitaa yetu ambayo miji tunataka tuikuze kwa gharama hiyo? Kwa hiyo nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri hebu ule mpango mlioutaja kwenye hotuba yenu ya kufanya utafiti kuona kama watu hawa wanaweza wakagharamia hiyo ni vema ukafanyika mapema. Hapa mimi ninashauri Kamati utakayoiunda itakwenda miezi sita lakini wananchi tayari walishajiandaa miaka mitatu iliyopita kuupokea umeme na ninaamini nchi hii ni kubwa mimi nikurahisishie tu kwa Jimbo langu la Kondoa Mjini. Jimbo la Kondoa Mjini ni Mji ambao unakua bado hauna ile hadhi kubwa ya kusema kwamba wananchi wenye kuishi hapa ni watu wenye uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mitaa ambayo naomba niitaje sasa hivi ni mitaa ambayo ipo vijijini kabisa ambapo hakuna mwananchi nikiangalia mmoja mmoja wa kulipa zaidi ya hiyo 300,000 au 600,000 kwa sababu asilimia kubwa watu hawa wanahudumiwa na mpango wa TASAF. Sasa najiuliza mtu unamsaidia kula asubuhi, mchana na jioni kwa kutumia TASAF anawezaje kuingiza umeme kwa hiyo pesa? Lakini sote tunakubaliana ukipeleka umeme kijijini maana yake unakwenda kuinua uchumi wa wanavijiji wale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshuhudia maeneo mengi ambayo mmepeleka umeme vijiji vile vimebadilika kabisa katika shughuli za kiuchumi, badala ya watu kulima wameweza kufungua viwanda vidogo vidogo, wameweza kufungua saloon na vitu kama hivyo. Kwa hiyo, kwa sababu nchi yetu ipo katika uchumi wa kati ni vema sasa mitaa hii tusiibague kwa kusema tuwafungue umeme kwa gharama kubwa kwa sababu kuwapelekea huduma ya umeme ni kuwasaidia kuwakwamua kiuchumi, kwa sababu nchi yetu ipo katika uchumi wa kati tunaamini sasa tutaendelea kuulinda huo uchumi wa kati kwa kuwapelekea wananchi umeme maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwa naona aibu sana ninapofanya ziara kwenye Jimbo la Mjini halafu unakwenda Kata nzima hata nguzo haina kwangu inakuwa ni shida sana. Tunaitaje Mji hali ya kuwa hakuna mwanga kuna giza wakati wote? Naomba niitaje hii mitaa ili Mheshimiwa Waziri ayachukue mambo haya yangu siyo mengi ni matatu tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ni huo mradi wa REA Kata ya Bolisa lazima ufike mwisho na wananchi wapelekewe umeme ili kupunguza kero kwa wananchi, jambo la pili ni kuiangalia hiyo Kata ya Suruke ambayo yenyewe Kata yote na mitaa yao hakuna hata nguzo iliyosimama kwenye ardhi ya Kata hiyo, maana yake siyo umeme tu hata nguzo haijasimama. Tuna mtaa wa Damai, tuna mtaa wa Kwantisi, mtaa wa Gubali, mtaa wa Hachwi, mtaa wa Chandimo, mtaa wa Serya, mtaa wa Dumi, mtaa wa Kwamtwara, mtaa wa Chemchem, mtaa wa Tampori, mtaa wa Ausia, mtaa wa Suruke, mtaa wa Guluma, mtaa wa Tungufu pamoja na mitaa ya Unkuku pamoja na Choyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa fikiria ni Jimbo lenye Kata Nane peke yake mitaa yote hii haina umeme na tunasema hii ni Halmashauri ya Mji. Mimi Mheshimiwa Waziri ninakuomba ndugu yangu hakikisha waelekeze REA wakawasaidie, ule mpango wa TANESCO wa kwenda kusema unakwenda kujaziliza, TANESCO yenyewe bajeti yao ni ndogo wakipata nguzo 20 hazifiki popote. Leo Mji unapanuka maeneo ya karibu ya Mji, TANESCO wanaweza wakamudu kwa hizo nguzo 30, 20, 40 lakini mtaa mzima hauna umeme, Kata nzima na mitaa yake haina umeme hawa wanahitaji wasaidiwe mradi wa REA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaambiwa kuna hii nini Peri-urban, tunaisikia Dodoma tunaisikia Dar es Salaam, tunaisikia Arusha kwenye miji yetu ya Halmashauri huko kwa kweli hatuna matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nina mashaka makubwa sana na kuwa na Halmashauri za Mji, leo mambo ya Halmashauri ya Mji yamekuwa ni ya kusubiri ninaogopa tutasubiri na huu umeme mpaka vijiji vyote vitakamilika. Kwa hiyo tutakuza vijiji tutasahau kuikuza mitaa yetu. Leo ukija kwenye maji Miji 28 tunaendelea kusubiri ukija kwenye tactic masuala ya barabara tunasubiri, ukija kwenye umeme tunaambiwa kuna huo mradi tofauti na REA ambayo tunajua ndiyo wanafanya vizuri sisi tunaendelea kusubiri! Hivi ni dhambi kuwa na Halmashauri ya Mji? Ninaunga mkono hoja na wala sina haja ya kushika Shilingi na nitaitikia ndiyo bajeti yao lakini wafahamu kilio hiki cha Mbunge mwenzao kinanisababishia mimi wakati mwingine nakimbia Jimboni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia Mpango pamoja na Bajeti hii ya 2022/2023. Kwanza niipongeze Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutekeleza vilivyo Ilani ya Chama cha Mapinduzi na kutuletea mpango ambao kwa kweli umekwenda kuwagusa wananchi wa maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri kuanzia mwanzo mpaka mwisho sijaona mahali pameelezea japo kwa ufupi Sekta ya Ardhi. Kwa hiyo, naomba angalau wakati Mheshimiwa Waziri anakuja ku-windup japo atuletee maelezo mafupi kuhusiana na Sekta ya Ardhi kwa sababu shughuli zote za kiuchumi zinafanywa kwenye ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia ardhi hii inaipa nchi kipato kikubwa sana, kwa sababu ardhi iliyopimwa ina uwezo wa kuchangia kipato kikubwa sana kwenye Taifa hili. Moja, wakati wa mauzo ya ardhi Serikali inapata fedha, pia wakati wa kodi ya viwanja na wakati wa malipo ya kodi ya majengo. Kwa maana hiyo, tupate japo maelezo kidogo tuone namna gani Wizara hii inakwenda kuweka umuhimu wa sekta ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya vizuri sana kwenye Sekta ya Ardhi. Leo Serikali imetoa mikopo kwa ajili ya halmashauri kwenda kupima ardhi zao. Halmashauri nyingi zimenufaika kwa mikopo ya Serikali. Mwezi huu tu Wizara ya Ardhi imeweza kukopesha halmashauri mkopo usio na riba wenye thamani ya shilingi bilioni nne kwa halmashauri nne. Kwa maana hiyo, sekta hii ni muhimu sana na Wizara inafanya vizuri sana kuhakikisha maeneo haya yanapimwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la Sekta ya Utalii tumeona namna gani watalii wameongezeka kutokana na filamu ya royal tour na tuna habari kwamba Zanzibar imejaa wageni, lakini hata Bara wamejaa wageni kutokana na royal tour. Sasa sisi kama Taifa tunatakiwa sasa katika mipango yetu ya ndani tuhakikishe ujio huu wa wageni wengi usikome na uendelee muda wote. Utaendelea vipi? Ni kwa sisi wenyewe kupanga mikakati yetu ya ndani kuanzia tunapoweza kumpokea mgeni anapoingia mpaka wakati anaondoka, kiasi kwamba wakati anaondoka atamani tena kurudi ama atamani kwenda kushawishi wageni wengine waje kuitembelea nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tunapaswa kutoa vikwazo vyote ambavyo vitakuwa ni kero kwa wageni wetu. Kwa hili naamini Wizara itafanya vizuri na itahakikisha kazi kubwa iliyofanywa na Mheshimiwa Rais itaendelea vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapoongelea Sekta ya Utalii katika nchi hii, ni sekta ambayo inachangia katika pato la Taifa zaidi ya asilimia 17. Ni sekta ambayo imetoa ajira zaidi ya wananchi wa Tanzania 1,600,000. Kwa hiyo, ni sekta muhimu sana. Kwa hiyo, sisi tunapoiongelea Wizara ya Maliasili, tunatakiwa tuongelee Wizara kwa umakini sana kwa kujua kwamba Wizara hii imebeba uchumi mkubwa wa Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mawazo yoyote ya mtu yoyote ambayo yanaenda kwenda kuudumaza utalii wetu tuyakatae kwa nguvu kubwa sana. Ukishateuliwa na Mheshimiwa Rais kwenye sekta hii, katika Wizara hii usitegemee utasifiwa kwa sababu Wizara zote zinawatetea wanadamu, wewe peke yako utakuwa unatetea wanyama. Kwa maana hiyo, hakuna nafasi ya kusifiwa, unachotakiwa kufanya ni kusimamia sheria kwa ajili ya kulinda urithi wetu ambao sisi tumerithishwa na Watanzania, watoto wetu na wajukuu zetu watatamani kwenda kuona hivyo ambavyo tumevitunza tukarithishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwenda Sekta ya Ujenzi. Kuna jambo moja hapa ambalo nataka Bunge lako liweke sawa. Tuna Ilani ya CCM ambayo imeandaliwa vizuri sana na viongozi wetu makini na nina uhakika Ilani ile ni Ilani bora sana na ikitekelezwa tunakwenda kumuinua mwananchi mmoja mmoja. Sasa katika ujenzi lengo la CCM ni kuhakikisha wanaendelea kujenga barabara ili kuwawezesha wananchi waweze kujijengea kipato chao na maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hii barabara ya Handeni inayokwenda mpaka Singida. Barabara hii nimepata mashaka kidogo, kwanza kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameitaja vizuri barabara hii. Amesema kwamba barabara hii ya kilomita 460 itaanzia Handeni – Kibrashi – Kibaya na kwenda mpaka kwa Mtoro, lakini katika Mpango wa Serikali pia umetaja kama alivyotaja Waziri wa Fedha, hii haina mashaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mgogoro unakuja kwenye taarifa ya Wizara ya Ujenzi, wao waliitaja kwamba inatokea Handeni – Kibirashi – Kijungu – Kibaya – Njoro – Ugoloti – Mrijo Chini – Dalai – Bicha halafu inarudi tena Chambalo inakwenda tena Chemba ndiyo iende kwa Mtoro halafu Singida, jambo hili ambalo haliwezekani. Ni kwamba barabara imezungushwa eneo moja lilelile ambalo nadhani Ilani ya CCM ambayo ndiyo ilitaka Serikali ijenge ile barabara, imeeleza vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Ilani ya CCM ukurasa wa 73 imetaja kwamba barabara hii itajengwa kuanzia Handeni - Kibirashi – Kondoa kwenda Singida wakifahamu kwamba, barabara hii ni barabara ya TANROAD ambayo ilikuwepo miaka mingi na ndiyo inafahamika. Barabara hii inatakiwa ijengwe kuanzia Handeni – Kibirashi – Mrijo Chini iende Dalai, iende Mondo, iende Bicha, iende Selya ikatokee kwa Mtoro ndizo hizo kilomita 440 zitatimia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango huu na nilikwenda kuonana na Naibu Waziri wa Ujenzi, yeye pia ana mpango wake, ambao mpango wake niliona unakata vijiji na mitaa mingi sana inaishia nyuma ya kijiji ambacho kinaitwa Dalai, halafu inakwenda Chemba halafu ndiyo inakwenda kwa Mtoro, Ilani ya CCM haijasema hivyo. Ilani ya CCM imesema barabara hii inakwenda Kondoa halafu ndiyo kwa Mtoro, halafu ndiyo ufupi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukitokea Kondoa kwenda Singida kwa njia ya Kwa Mtoro haizidi saa moja na robo, lakini kwa namna Wizara ilivyosema, ukitokea Kondoa kwenda Singida kwa barabara hii wanayoisema ni zaidi ya masaa manne. Kwa hiyo, utaona kwamba barabara hii inatakiwa Mheshimiwa Waziri akija, atamke ili wananchi wa Dalai, Mondo, Bicha na Selya wajue kwamba mpango wa CCM kwenye Ilani yake utatekelezwa kama namna Ilani ilivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, halafu wakati vikao vya chama vinapendekeza barabara hiyo ni kama vilijua. Barabara hii ndipo Mradi ule wa Bomba la Mafuta unapopita. Sasa ukiikwepesha barabara hii maana yake shughuli nyingi za uchumi zitakwama. Kwa maana hiyo, barabara hii ni muhimu kwa sababu kuna bomba la mafuta na kuna kituo kikubwa ambacho kitajengwa katika Kata ya Selya. Kwa maana hiyo, kutokuitendea haki barabara hii kutasababisha kwamba mengi kutoenda. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu barabara hii ya TANROADS ndiyo barabara ambayo itapokomea hapo Selya itakuwa inaelekea Usandawe ambako ndiko huko kwa Mtoro. Hapa inapokomea ni barabara ya TANROADS ambayo inakwenda kuunganisha na Hanang’. Tunafahamu Hanang’ ni wakulima wazuri wa zao la ngano. Sasa kuzunguka kwenda Moshi mpaka Tanga kwenda Dar es Salaam au Singida kuja Dodoma – Morogoro watakuwa wanatembea kilomita zaidi ya 600, lakini kwa kupitia Kondoa ni hizi hizi kilomita 460.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, naunga mkono hoja, lakini Mheshimiwa Waziri akija atuelezee kwamba CCM ilivyopanga kwenye Ilani ndicho kitakachofanyika kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)