Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Alexander Pastory Mnyeti (6 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Pia nitumie nafasi hii kuwashukuru Wanamisungwi kwa kunipitisha bila kupingwa na Madiwani wangu wote 27 na hatimaye sasa tupo humu kwa ajili ya kuwatumikia Wanamisungwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mengi yamesemwa, mchango wangu nitajikita kwenye mambo matatu, jambo la kwanza ni kweli kwamba Taifa letu msingi wake mkubwa ni kilimo na kwa sababu hiyo tuna kila sababu ya kuelekeza nguvu kubwa kwenye kilimo tuwasaidie wakulima wetu hawa ili waweze kuleta tija kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mashamba makubwa ambayo Serikali iliwapa wawekezaji ili wayaendeleze, lakini kwa masikitiko makubwa mashamba hayo mengi yametelekezwa na hao wawekezaji na hakuna kinachoendelea. Sasa niombe Wizara ya Ardhi, kama kuna namna yoyote ya kufanya mashamba hayo ama yarudi kwa wawekezaji wengine ama yarudi kwa wananchi ili wananchi waweze kuzalisha. Mashamba hayo wawekezaji unakuta mwekezaji mmoja anamiliki mashamba ekari 20,000, wengine ekari 50,000, wengine hivi, lakini ukiangalia uendelezaji wa mashamba hayo ni asilimia nne hadi 10, eneo lingine lililobaki lote liko wazi halilimwi na wananchi wanashangaa Serikali inashangaa na mwekezaji anashangaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama kweli lengo letu ni kuzuia kuagiza vitu nje ya nchi, hebu basi tutengeneze mazingira ya kuzalisha hayo mashamba yafanye kazi ili basi tuongeze pato la Taifa kwa namna hiyo, vinginevyo tutaendelea kuagiza choroko, ngono, nyanya, vitunguu, kila kitu tunaagiza kutoka nje lakini mashamba tunayo hayafanyiwi kazi. Ukienda kule Bassutu kuna mashamba ngano, tunasema tunaagiza ngano, wakati mashamba tunayo lakini hakuna anayeyalima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kweli tuko serious na hii mipango, otherwise mipango ya kwenye karatasi kama kweli tunataka tutoke hapa tulipo, yako mambo makubwa ambayo tunatakiwa tuchukue hatua ili basi tuweze kutoka hapa tulipokwama. Mashamba yametekelezwa, nenda Lotiana mashamba makubwa yametekelezwa. Leo Tanzania bado tunaagiza nyama kutoka nje ya nchi. Hii mipango, ni kweli ni mipango mizuri lakini utekelezaji wake mbona tunakwama, mashamba yametekelezwa, hatuendi kwenye kugota kwenye pointi ya kwamba tunatokaje kwenye hili tatizo lililokwamisha, haya makaratasi ni mazuri kwa sababu yameandikwa na Professors, ma-PhD holder lakini utekelezaji wake. Nazungumza utekelezaji wa namna gani tunakwama hapo tulipokwamia. Kwa hiyo, naomba hili niishauri sana Serikali kama kweli tuko serious hebu mtoke hapa tulipokwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, tumeanzisha viwanda vingi sana kwenye Taifa letu kwa muda mfupi, hongera sana Serikali kwa kazi hii nzuri. Hata hivyo, nasikitika kukujulisha kwamba viwanda hivi baada ya muda vitakufa vyote, kwa sababu hatuna malighafi yakuendesha hivyo viwanda, tunazalisha wapi? Unaniambia tunaanzisha viwanda ni kweli kule Iringa viwanda vya kuchakata mbao, lakini viwanda hivi miti iko wapi? Miti iko wapi, viwanda vinaanzishwa kule Misungwi, vinaanzishwa Kahama, vinaanzishwa wapi vya kuchakata pamba, pamba iko wapi? Tuwahamasishe wakulima wetu walime, tuwawezeshe pembejeo za kilimo walime. Hii Habari ya kumfurahisha mkuu wa nchi kwamba tunaanzisha viwanda, halafu baada ya miaka sita vimekufa, hii nataka niseme tutashindwa na tunashindwa very soon kwa sababu hatuwahamasishi wananchi kulima, hatuwatengenezei mazingira mazuri wananchi wetu waweze kulima, waweze kupatiwa pembejeo za kilimo, matrekta na kila kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kiwanda chetu cha mbolea; leo mbolea tunanunua 60,000 mpaka 55,000 kwa mfuko wa kilo 25 mpaka 50. Sasa tuna Kiwanda chetu kule Minjingu, kiwanda peke kwenye Taifa letu, lakini Serikali ni kama wamekipuuza, bado wanaagiza mbolea nje ya nchi, inafika mbolea hapa kwa 50,000 mpaka 60,000, lakini kile kiwanda kipo, Serikali ikikiwezesha kidogo tunaweza tukanunua mbolea 20,000 mpaka 15,000 kwa sababu tuna uwezo wa kutengeneza mbolea yetu wenyewe kwenye Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka niwaambie….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya katika Taifa letu, hususan katika Jimbo letu la Misungwi, kwa sababu mambo mengi tumeyaona Mheshimiwa Rais ameyafanya katika sekta za afya, elimu na maeneo mengine. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza ambalo nataka niishauri TAMISEMI. Mheshimiwa Waziri anafanya kazi nzuri sana na wasaidizi wake. Kwa bahati nzuri anafahamu kwamba mimi nimefanya kazi Serikalini, kwa hiyo Mawaziri wajanjawajanja wote nawajua na wasanii wote nawajua kwa sababu tumefanya kazi kwa pamoja kwa muda mrefu, lakini nataka niseme kwamba Mheshimiwa Angellah Kairuki ni Waziri imara sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, iko changamoto kubwa ambayo Waheshimiwa Wabunge wamejaribu kuieleza sana. Hii kero kusema kweli hata jimboni kwako najua ipo, yako maboma ambayo wananchi wetu wameyajenga wakafikia kwenye maeneo ya lenta na wengine wakamaliza maboma. Maboma hayo yametelekezwa miaka kumi, mengine miaka 15, lakini Serikali kupitia nyaraka mbalimbali ilizokuwa ikizitoa kule vijijini ilikuwa inahamasisha wananchi wajenge yale maboma, wakishamaliza Serikali imalizie. Hata hivyo, Serikali haijamalizia hayo maboma. Tunaomba sana kwa Mheshimiwa Waziri, ziko zahanati wananchi wamejenga, yako madarasa wananchi wamejenga, wanaomba yakamilishwe.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, ziko halmashauri nyingi sana ambazo hazipeleki asilimia 40 vijijini. Pesa zote zinaishia pale halmashauri wanatumia wanavyotaka asilimia yote 100 na haiendi kule vijijini. Tunaomba sana Mheshimiwa Waziri alione hili na alifuatilie kwa karibu sana kwa sababu yamekuwa ni malalamiko ya Wabunge wengi na wanahitaji kujua asilimia 40 zina matumizi gani kule vijijini.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, kule Misungwi naishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mama Samia na usimamizi wa TAMISEMI nilijengewa hospitali ya wilaya, nashukuru sana, zaidi ya majengo kumi yameshakamilika, lakini majengo haya hayana vifaatiba. Mheshimiwa Waziri akiacha kuyapelekea vifaatiba na mwaka huu maana yake yatabaki kuwa white elephant kwa mwaka mzima hayafanyi kazi na mwisho wa siku yataanza kuchakaa.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, namwomba sana Waziri amthibitishe Mkurugenzi wangu awe Mkurugenzi rasmi. Tumekaa naye miaka mitatu amefanya kazi nzuri. Mapato tuliyokuwa nayo toka bilioni mbili kwa mwaka sasa tuna bilioni nne, lakini mwisho wa siku watu wazuri kama hawa huwa hawataki kuwathibitisha, wanawahamisha wanawapeleka maeneo ya wajanja, sisi tunabaki tunatoa macho. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri huyu Mkurugenzi ametufanyia kazi ya heshima Wanamisungwi, tunamhitaji, tunaomba wamthibitishe ili aweze kufanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Nitazungumzia mambo matatu. Jambo la Kwanza, mwaka 2010 wananchi waliokuwa wanaishi karibu na ile Barabara ya kutoka Geita kwenda Usagara walilipwa fidia zao, lakini wananchi kama tisa hivi wakasalia wakidai jumla ya shilingi milioni 30. Tangu mwaka 2010 mpaka leo wananchi hao wanadai milioni 30, wanaidai Serikali, haya ni mambo ya aibu, milioni 30 kudaiwa na wananchi maskini, waliowanyang’anya maeneo yao wakapitisha barabara. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri hilo alichukue. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, kule Misungwi tuna hili Daraja la Kigongo kwenda Sengerema, daraja hili wale wakandarasi walipewa tender hiyo na sasa wanaendelea vizuri na ujenzi, lakini cha kusikitisha wamevamia milima ya wananchi wanaponda kokoto wanachukua bila utaratibu bila malipo ya aina yoyote. Mheshimiwa Rais alivyopita pale jambo hili liliibuliwa na wananchi na Mheshimiwa Rais akaagiza twende tukalishughulike. Tumekwenda kushughulika na jambo hilo tukaonyeshwa dharau ya juu, akaja Mheshimiwa Waziri tukamweleza jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasikitika kumjulisha kwamba tangu ameondoka hakuna kilichofanywa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa Mheshimiwa Waziri, yeye ndiye Waziri wa Ujenzi, anakuja pale anatoa maelekezo kwa wakandarasi aliowapa tender mwenyewe lakini bado watu hao hawafuati alichowaagiza. Hii nayo ni aibu kubwa. Nitoe ushauri kwa Mheshimiwa Waziri, tupunguze sana kutoa tender hizi za ujenzi kwa wakandarasi wa Kichina wana dharau sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tunashindwa kutengeneza wakandarasi wetu wenye nguvu ndani ya nchi yetu, tunashindwa nini kuwawezesha watu wetu wa ndani ili waweze kujenga barabara zetu na miradi mingine. Pale kwenye ule Mradi wa Kigongo – Busisi wale Wachina wanatengeneza, lakini hakuna mkandarasi mwenza wa Tanzania anayeangalia nini kinajengwa ili keshokutwa tujenge na sisi wenyewe madaraja yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumewaacha wale Wachina, wanajenga wanavyotaka wenyewe, wakijenga chini ya kiwango hakuna anayejua, wakiweka mawe badala ya cement hakuna anayejua, mwisho wa siku tunakabidhiwa vitu hivi vikija kuanza kuharibika hakuna anayeweza kuvikarabati mpaka tuwatafute Wachina wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama kweli tupo serious, otherwise nataka nitoe mfano mmoja, waulizeni Wazambia walifanywa nini na Wachina. Waliamua kukabidhi nchi yao kwa Wachina, leo tunavyozungumza kila kitu kimekamatwa na Wachina. Sasa na sisi tunarudi kulekule, madaraja yote Wachina, barabara zote Wachina, makalvati Wachina, majengo yote Wachina, kila kona Wachina, kila mtu Mchina sasa tunafanya nini? Hivi kweli hatuna, bahati nzuri Mheshimiwa Waziri alikuwa Mwalimu wa Chuo Kikuu pale, hivi hajafundishwa mainjia vijana wetu wa Kitanzania wanaoweza kujenga madaraja. Sasa kama hajafundisha maana yake tunapotezeana muda sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hilo Waziri aliangalie, lakini hapo hapo kwenye hilo daraja kuna vijana wetu wameomba kazi, wanaozunguka maeneo hayo, wanaoishi katika maeneo hayo, mpaka kesho hakuna hata mmoja anayepewa kazi pale. Wale Wachina wana watu wao, tunaambiwa kwamba ile kampuni ya Kichina imeingia hapo miaka ya 70 au 60 kwa hiyo wana watu wao sijui wanawatoa wapi kuja kufanya kazi pale Misungwi, lakini wale watu wa Kigongo Ferry pale hawapati kazi, hata ndogo ndogo zile hawapewi. Mheshimiwa Waziri alikuja Misungwi nikamwambia jambo hili, lakini tangu ameondoka hakuna kilichofanyika. Sasa kama ni mambo ya porojo, basi tuendelee kupiga porojo, mwisho wa siku hakuna kinachofanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu, nizungumzie kuhusu Shirika la Ndege. Sisi kule Mwanza unaingia kwenye mtandao unafanya booking, tunaipongeza Serikali kwa kununua ndege nyingi za kutosha, lakini unaingia unafanya booking unaambiwa ndege imejaa. Wakala anakwambia hebu subiri nikufanyie sarakasi upate tiketi ya kwenda Dar es Salaam, anafanya sarakasi yaani wakala wa tiketi naye amekuwa bosi sasa hivi, anafanya sarakasi unapata tiketi ya bahati nasibu, ukiingia kwenye ndege hakuna watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yaani tunahujumiana sisi wenyewe kwa wenyewe na huu mchezo Mheshimiwa Waziri nataka nimwambie, huu mchezo upo kwenye Wizara yake. Unafanya booking hakuna nafasi, ukiingia kwenye ndege ukibahatisha hukuti watu kwenye ndege bombardier ile inasafiri na watu 15 watu 20, lakini kwenye kutafuta unaambiwa tiketi zimejaa, tafuta usafiri mwingine. Hapa tunamkomesha nani? Ni nani tunamkomesha, tunajikaanga kwa mafuta yetu wenyewe Watanzania, ndege hizi mwisho wa siku zitakuwa ni za kupigia picha, watu wanatafuta tiketi, tiketi hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hilo hilo, ukifanya booking kutoka Dodoma kwenda Dar es Salaam unaambiwa tiketi laki tano. Ukiangalia kwenye ile ndege nyingine sitaki kuitaja jina hapa unakutana na tiketi ya laki mbili, halafu ukilipa hiyo laki tano ukiingia kwenye ndege hakuna watu, kwa nini Waziri asiweke bei reasonable ili watu wengi wa kawaida wapande ndege na ndege zetu zijae. Tunamhujumu nani? Tunahujumiana sisi wenyewe Watanzania, mwisho wa siku hizi ndege zitakuwa ni ya kupigia picha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, TANROADS Mwanza unaweza ukazunguka nchi nzima ukitoka Dodoma hapa utaenda vizuri, utaenda vizuri ukishaona kibao kinasema, sasa unaingia Mkoa wa Mwanza unaanza kukutana na sarakasi za mabonde, viraka, mabarabara yasiyoeleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, maeneo mengine wanataka lami na sisi tunataka hayo hayo mabonde yadhibitiwe TANROADS Mwanza kuna shida gani? Kwa nini ukifika Mwanza tu ndio unakutana na mabonde kuinama unaingia kwenye majaluba mule mule kwenye lami kuna majaluba mule mule kuna matuta. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri hebu iangalie vizuri Mwanza kuna shida gani Mwanza ni mkoa mkubwa huo ndio ukweli, haya mabonde mabonde ni aibu tunatiana aibu. Kama hatuwezi kutengeneza barabara basi tuseme hatuwezi kutengeneza barabara, lakini sio kila siku tunaziba viraka mara kiraka hiki kimepasuka hapa, mara kinazibwa hapa. Hizo gharama mara mia tano zikatengeneze mabarabara mapya huko Kusini kama hamuwezi, kwa sababu imeonekana kama ni deal. Kila mwaka mnatengeneza mabarabara hii ni deal ya watu kila siku mnaziba viraka, kwa sababu ya deal kila siku deal. Pale Wilayani kwangu Misungwi kuna kilometa karibia 20 kila mwaka TANROADS wanatengeneza barabara kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwangu naona huu ni usanii na tunaiba pesa za watu. Jambo la mwisho limesemwa hapa kwamba, daraja la Busisi lisiendelee kujengwa mpaka ipatikane certificate ya mazingira. Yaani unaaga kwa mumeo kwamba nakwenda kazini kuja kusema kitu kama hicho kwamba, daraja lisijengwe eti kwa sababu hakuna certificate ya mazingira! Sisi tunasema hivi mazingira ni ya kwetu, daraja ni la kwetu, ziwa ni la kwetu, kila kitu ni cha kwetu tunahitaji daraja lijengwe na kwa wakati na likamilike na tunahitaji kwa muda mfupi. Naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Nianze kwa kupongeza Wizara kwa kazi nzuri wanayofanya chini ya Waziri Bashungwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mchango mfupi sana kwenye Wizara hii ya Michezo, jambo la kwanza ni makato yanayofanywa na Serikali baada ya mechi. Tunafahamu wote kwamba kuandaa timu au kuandaa mchezo ama mchezo ni gharama kubwa, lakini inasikitisha sana baada ya mechi, Serikali mmekuwa mkivamia hayo mapato na kuanza kuyakatakata vipande vipande. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapoandaa mechi tatizo la Serikali wanakwenda kuangalia nini kimepatikana siku ya mechi. Hawaangalii umetumia shilingi ngapi kuandaa hiyo mechi. Tafsiri yake ni kwamba wanakuja wanakatakata mpaka wanakula mtaji halafu kesho timu zinashindwa kuandaa mechi. Serikali haijui mchezaji ili ahudhurie mechi moja anahitaji kula, kuvaa, kutibiwa, kunywa maji, kwenda mazoezi na kufundishwa na mwalimu aliyebobea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, yote hayo Serikali hawayajui na hawataki kuyasikia. Siku ya mechi utawaona wako getini TRA wanakata asilimia 18, Halmashauri wanakata asilimia 10, BMT wanakata asilimia tatu, pasipo kujua umewekeza shilingi ngapi mpaka kufika siku ya mechi. Sasa kwa mfano, unatumia shilingi milioni nane kuandaa mechi moja, halafu getini unapata shilingi 2,100,000. Lakini fedha zote hizo Serikali inaziangalia na inakwenda kuzikata pasipo kujua umetumia shilingi ngapi kwenye kuandaa hiyo mechi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naona huu ni uonevu na kwa stahili hii hatuwezi kuendeleza mpira wa miguu kwa namna yoyote ile, vinginevyo kama tunapiga story ili muda uende hakuna, haitawezekana. Hii kuandaa timu imekuwa ni kama watu wanapiga story sio jambo rahisi kama tunavyofikiria. Wachezaji hawa wanakula, wanatibiwa, wanaumwa, ankle, magoti, sijui visigino vimefanya nini. Ukimtibu mpaka kumpeleka kwenye mechi ni gharama kubwa, lakini inasikitisha sana wakati unafanya hayo yote Serikali haipo. Unawatibu wachezaji Serikali haipo, unalipa kocha Serikali haipo, Serikali inakuja kuonekana siku ya mechi inataka asilimia 18. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri akaliangalie hili vizuri akae na wenzake muone mnawezaje kusaidia hivi vilabu ambavyo vinasuasua havina hata shilingi ya kuendesha huu mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, tunampongeza sana Azam kwa udhamini mkubwa wa mwakani ambao ameufanya, lakini si tu mwakani, Azam hata mwaka huu, mwaka jana, mwaka juzi walau chochote ameweka kwenye mpira huu wa miguu na tayari ameanza kwenye michezo mingine kama ngumi, netball na michezo mingine. Tunampongeza sana huyu mwekezaji, mwekezaji mzawa tunaomba aendelee kufanya hivi kwa sababu ndio njia pekee ya kuinua soka la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimuombe Mheshimiwa Waziri kuna mdhamini mwingine anaitwa Vodacom ambayo ligi inayokwisha sasa ambayo bado mechi tatu, nne kuisha. mdhamini huyu ndio mdhamini mkuu kwenye ligi ya Vodacom. Nasikitika kukujulisha mpaka sasa hajawahi kuweka hata shilingi 10 pamoja na udhamini huo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kila vilabu vinapouliza jambo hili limekuwa likipigwa chenga. Mheshimiwa Waziri ingilia kati, saidia hivi vilabu vipate haki yao hata kama anaacha, lakini haki ya vilabu vimepatikana ili waendelee na mpira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, najua hili linaweza likachelewa sana kueleweka lakini ndio ukweli, tukizungumza siasa ya mpira katika nchi hii tunazungumza siasa ya Simba na Yanga, lakini Simba na Yanga hawana msaada wowote kwenye kuunda timu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tusisubiri matokeo ya timu ya Taifa ifanye vizuri halafu akili zetu na nguvu zetu zote tumeelekeza kwenye Simba na Yanga. Simba na Yanga hapa wote tunajua ina nguvu kubwa, ina political mileage kila mtu anashabikia na wengine tuko humu tunashabikia ni sawa kabisa. Lakini tusiulize kwa nini timu yetu ya Taifa haifanyi vizuri, ni kwa sababu akili zetu na nguvu zetu zote tumeelekeza kwenye Simba na Yanga, tumesahau vilabu vidogo ambavyo ndivyo vyenye mchango kwenye timu yetu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikutolee mfano mmoja, ukiongelea habari ya Simba, juzi Simba wamecheza robo fainali ya Kombe la Afrika tunawapongeza sana. Lakini nikutolee mfano mmoja kule, lineup ya Simba wachezaji watatu tu ndio Watanzania golikipa, namba mbili na namba tatu basi. Namba nne Mkenya, namba tano Ghana, namba sita Mganda, namba saba Mozambique, namba nane Zambia, namba tisa Congo, namba 10 Zambia, 11 Rwanda. Huwezi kupata timu ya Taifa kama wachezaji wa Simba na Yanga wote lineup wanatoka nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda kule Yanga, mara sijui Tusiletusinde, mara Tunombetunombe, mara Mandama, sijui vitu gani. (Kicheko)

Nataka nikuambie tunajenga Simba na Yanga kwa nguvu kubwa lakini hatujengi timu ya Taifa kwa sababu tunapoita wachezaji wa timu ya Taifa hatuwaiti wale kwa sababu wanatoka nje ya Taifa letu. (Makofi)

Sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri kama kweli tunataka tujenge msingi wa mpira katika nchi hii, haya mambo ya Simba na Yanga tungeweka baadaye ikawa ni second option. Kipaumbele ikawa ni wachezaji wetu wa kitanzania wazawa, ambao tunaweza tukawatumia kwenye timu yetu ya Taifa na wakaleta tija kwenye nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kwenye Taifa letu kila mtu ni Simba ama ni Yanga; anayejua mpira yuko Simba ama Yanga. Simba Yanga, Simba Yanga, Simba Yanga nonsense, hatuwezi kila saa hapa tunaongelea mambo ya Simba Yanga, Simba Yanga, which is Simba and Yanga. Kama tunazungumza habari ya maendeleo ya mpira ya miguu kwenye Taifa letu, Simba na Yanga ziwe second option.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha kwanza, tuunde wachezaji wetu wa kizawa wanaoweza kuleta tija kwenye Taifa letu, tofauti na hapo tukiendelea kupiga hizi story tutapoteza muda na hakuna tutakachopata. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii. Nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri anayoendelea kuifanya katika Taifa letu. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Serikali kwa ujumla kwa kazi na namna ambavyo wanamsaidia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo matatu ya kuzungumza kwenye Wizara hii. Jambo la kwanza ni namna ambavyo bado tunaendelea kuagiza bidhaa mbalimbali kutoka nje ya nchi ambazo tuna uwezo wa kuzizalisha ndani ya nchi yetu. Hili nimekuwa nikilisema sana. Kwa bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wakati anaeleza hapa asubuhi amejaribu pia kuelezea jinsi ambavyo bado tunaagiza mafuta ya kula, bado tunaagiza ngano, tunaagiza vitunguu, na tunaagiza vitu vingi sana kutoka nje ya nchi, ambapo vitu hivi tuna uwezo wa kuvizalisha wenyewe ndani ya nchi yetu kupitia mashamba yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikishauri sana, yako mashamba makubwa ambayo walipewa wawekezaji miaka ya nyuma wayaendeleze. Wawekezaji hawa wameyatelekeza mashamba haya. Unakuta mtu amepewa shamba ekari 40,000, ekari 30,000, lakini kwenye ekari 40,000 huko anatakiwa alime ngano kwa asilimia 100, halimi hiyo ngano. Ekari 40,000, anaishia kulima ekari 3,000 au 2,000. Ekari 38,000 anatelekeza, ameacha. Unakuta kwenye shamba hilo la ekari 40,000 yeye mwenyewe anakodisha wananchi wanaozunguka maeneo hayo ekari 5,000, shamba linalobaki lote ameliacha. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, nenda kwenye mikoa mikubwa kama Morogoro, Tabora na Mwanza, mashamba yametelekezwa. Kule Misungwi kuna shamba la vitunguu, scheme ya umwagiliaji nzuri kabisa ambayo Mwisraeli alitutengenezea vizuri, sasa imetelekezwa, hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri, haya mashamba Watanzania wako tayari kuyaendeleza, na hata kama sio Watanzania, wako wawekezaji wenye uwezo na vision ya kuendeleza haya mashamba, na wana nguvu, wana mtaji wanaweza kuwekeza. Hao wawekezaji ambao hawawezi kuwekeza hayo mashamba, watupishe tuweke watu wengine. Sasa hili limekuwa kama wimbo, tumekuwa tukilisema sana, lakini hatuoni Serikali ikizichukua hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Kanda ya Ziwa na Mwanza kwa ujumla tunahangaishwa sana na kitu kinachoitwa mfumuko wa bei. Bidhaa za Viwandani zimekuwa zikipandishwa bei na wafanyabiashara na zinawaumiza watumiaji wadogo wadogo kule vijijini. Unakuta kitu kama nondo, milimita kumi sasa hivi ni shilingi 18,000 mpaka 20,000, mwingine anauza shilingi 21,000 au shilingi 22,000, lakini ni kuanzia shilingi 18,000 mpaka shilingi 22,000. Nani anayedhibiti hii bei ya nondo kule kwa mtumiaji Busongo, Nunduli, Serengeja mpaka Mwaulile? Kwa sababu mtu anajiamulia kutengeneza bei yake anayoitaka mwenyewe, anakwenda kuuza sokoni, na anayeumia ni mwananchi wa mwisho kabisa kule kijijini ambaye bei hi inamuathiri moja kwa moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo asubuhi tulikuwa tunazungumza hapa habari ya Tanga Cement. Sisi kanda ya ziwa hatuna kiwanda cha cement. Tunategemea sana Tanga Cement ambao ndiyo majirani wetu wa karibu kutuletea kule cement kule Tanga. Nimejitahidi kuangalia kwa nini hii kelele imetokea pale asubuhi? Nilichojifunza ni mambo matatu makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanga katika hali hiyo inayoendelea sasa hivi, ile deposit ya Tanga ambayo inachimbwa sasa hivi, inakwenda kuwa machimbo, kwa sababu watu watachimba ule mzigo, watapeleka Dar es Salaam kwa ajili ya cement. Kwa kuwa mahitaji ya Dar es Salaam ni makubwa sana, maana yake huyu mwekezaji anayetaka kununua kile kiwanda atawekeza kule nguvu zaidi ya kwenda kuchimba material na kupeleka Dar es Salaam kwa ajili ya production.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo naliona hapo, kwa nini tunashindwa kuweka wazi jambo hili? Kwa sababu viwanda hivi ni miongoni mwa viwanda ambavyo vilikuwa ni vya Serikali. Kule Tanga kuna viwanda viwili vya chuma ambavyo wawekezaji wameshindwa kuviendeleza na Serikali imevichukua. Ukienda kule Moshi kuna viwanda vya mbao na miti, wawekezaji wameshindwa kuviendeleza, Serikali imevichukua. Halikadharika Mwanza, halikadharika Arusha. Sasa najiuliza swali dogo tu, kwa nini hiki kiwanda, kwa masharti hayo hayo ambayo walipewa mwaka 1997, kwa nini hiki kiwanda kisirudi Serikalini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa wawekezaji ambao tuliwapa kwa nia njema wameshindwa kukiendesha kiwanda na kukiendeleza, wamefilisika, kama mlivyofanya Wizara ya Uwekezaji kuchukua vile viwanda vya wengine kupitia Msajili wa Hazina, kwa nini msifanye hivyo hivyo kwenye kiwanda hiki, mkarudisha Serikalini, halafu Serikali ikamlipa huyo mwekezaji aliyeshindwa kuendeleza, halafu ikatafuta mwekezaji mwingine ili kupunguza hizi kelele ambazo zimekuwa zikiendelea katika Taifa letu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu nililoliona, tutakaporuhusu kiwanda hiki kimilikiwe na mtu huyo huyo mmoja, kwa sababu tunafahamu viwanda vikubwa katika nchi hii viko vitatu. Kiwanda hiki cha Tanga, Twiga pamoja na Dangote, washindani wakubwa wawili sasa ukishajumlisha hicho kiwanda kikawa kitu kimoja, tafsiri yake ni kwamba, ushindani hautakuwepo, kwa sababu huyu mtu atakuwa anajipangia bei anavyotaka yeye. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bei anayoiamua yeye; leo tunanunua cement kule Mwanza shilingi 24,000 mpaka shilingi 25,000. Tutakapompa dhamana ya kumiliki na kiwanda kingine kiwe kimoja, tafsiri yake ni kwamba, akiamka akasema bei ni shilingi 40,000, hakuna wa kushindana naye kwa sababu ndiye mwenye viwanda vikubwa kwenye nchi yetu. Sasa huu ushindani tutaufanyaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba jambo hili Wizara iingilie kati, ione namna ambavyo inaweza ku-rescue situation hii ili sisi watumiaji wa mwisho kule chini kwa wananchi, tuweze kutumia gharama nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, ajitahidi sana yeye na Wizara yake kulinda wawekezaji wa ndani. Kumekuwa na changamoto nyingi sana. Wawekezaji hawa wa ndani wanapata misukosuko midogo midogo huko kwenye zile taasisi za Serikali. Shida ni kwamba, Mwafrika ukipata hela, unaulizwa maswali milioni moja kuliko angepata hela mtu mwingine ambaye sio Mwafrika. Yaani ni kwamba, kuna watu, kikundi kidogo kimejimilikisha fedha nchi hii, kiasi kwamba akija mtu mwenye hela mpya, maswali atakayoulizwa ni mengi kuliko uwekezaji alioufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mtu aliingiziwa fedha, shilingi milioni 500 kutoka kwenye akaunti ya Mheshimiwa Kingu, maswali atakayopigiwa na Benki Kuu, ni afadhali akaingiziwe hiyo milioni mia tano akiwa Uganda. Utaulizwa fedha inatoka wapi? Yaani hata wao hawajui fedha inatoka wapi. Fedha huwa inatoka benki, kwenda benki. Ukinikuta na fedha nyumbani kwangu, hapo chukua hatua, lakini kama Mheshimiwa Kingu ameingiza fedha kutoka benki kwenda benki, unauliza maswali gani, kwamba fedha inatoka wapi? Fedha huwa inatoka benki inakwenda benki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana, wawekezaji wa ndani, watu wanajitahidi sana kuwekeza ndani ya nchi yao, lakini vikwazo na ukiritimba umekuwa ni mwingi sana, kana kwamba hawana uwezo wa kuwekeza kwenye Taifa lao. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri hilo nalo ulitazame kadri inavyowezekana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia kwa kazi nzuri na kubwa anayoendelea kuifanya kwenye taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina barabara ambayo imesemwa kwenye ilani ya mwaka 2000, ikasemwa kwenye ilani ya mwaka 2005, ikasemwa kwenye ilani ya mwaka 2010, ikasemwa 2015, imesemwa 2020, na barabara hii haikuwahi kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Waziri Mbarawa, kwa kuwasikia wana misungwi, kwamba barabara yao ya Ng’wanangwa – Misasi – Kahama sasa inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami. Nitumie nafasi hii kwa niaba ya wana misungwi kukushukuru sana Mheshimiwa Waziri, kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwamba barabara hii sasa inakwenda kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ina faida nyingi na ndiyo maana faida hizi zimepelekea sasa Serikali kwenda kuijenga kwa kiwango cha lami, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Unajua tumekuwa tukimshukuru Mheshimiwa Rais, wengine wanahisi tunajipendekeza. Kama barabara imeshindwa kujengwa miaka yote hiyo Mama Samia amekuja kujenga kwa nini tusiseme ahsante? Tunashukuru sana, wananchi wa Misungwi wanashukuru na tutaendelea kushukuru sana kwa sababu Rais, huyu ameamua kuijenga barabara hii na tayari; juzi nilikuwa na kikao na Mheshimiwa Waziri, amepiga simu nikiwepo kuagiza tenda itangazwe wiki ijayo, tunashukuru sana. Kwa niaba ya wana Misungwi tunashukuru sana kwa habari hiyo. Kwa kweli tuna Imani kubwa sana na wewe Profesa na kazi hii tuna imani sasa wiki ijayo barabara inakwenda kutangazwa na mkandarasi apatikane mwadilifu na barabara iende ikajengwe ili wana misungwi waweze kupanua uchumi kwenye wilaya yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nataka nishauri. Tuna miji mikubwa ambayo inayokua kwa kasi, Mheshimiwa Waziri anaifahamu, na tumekwisha omba habari ya taa hizi za barabarani. Tuna miji yetu kama ya Misasi, Mbarika, Misungwi, Igongwa, Usagara tupate taa za barabarani ambazo zinabadilisha hata ile sura za miji yetu ambayo inakuwa kwa speed.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo pia ni siku ya kutoa shukrani zetu tu. Wana misungwi kila tulipokuwa tukiomba mambo haya yanafanyika. Fidia ya watu ambao barabara ilipokuwa inajengwa kutoka Usagala mpaka Geita wamelia kwa muda mrefu lakini leo watu hao tayari wamekwishapewa fidia yao, tunaishukuru sana Serikali hii. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri, kwa kweli tunakushukuru sana lakini pia tukushukuru sana, juzi tumesaini mkataba wa ujenzi wa kivuko kipya cha kutoka Mbarika mpka Buyagu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tusiposhukuru kwa haya sijui tusubiri vitu gani ili tuweze kushukuru? Kila ambacho tumeomba Serikali ya awamu ya sita mmetekeleza. Tumeomba fidia mmetupa, tumeomba barabara mmetupa, tumeomba kivuko mmetupa, tukimshukuru Mheshimiwa Rais, mnasema tunajipendekeza; tufanye nini sasa zaidi ya hayo? Kwa sababu yote tuliyokuwa tunaomba, yote tuliyohitaji yafanyike Mheshimiwa Rais amekubali kuyafanya, zaidi ya hapo tufanye nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Serikali na muendelee kuchapa kazi kwa style hiyo kwa sababu sisi kwa niaba ya wananchi wetu tunaona mnayoyafanya na tunaamini kila tunayoyaomba mnaendelea kuyatekeleza kadri ya mwongozo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri anisikilize kwa makini sana kuhusu bandari. Sisi ni wanasiasa lakini pia tunafanya na vibiashara vidogo vidogo. Tunapata adha kubwa sana tunapoagiza mizigo yetu kupitia kwenye Bandari yako ya Dar es salaam. Mimi ninaishi Mwanza, tunapoagiza mizigo kutoka China, Japan na maeneo mengine, mzigo unaweza ukakaa bandarini hata mwezi mzima haujapata mzigo wako. Hiii ni aibu, kama mimi Mtanzania nachukua muda wote huo hao wa nchi jirani wao wana maisha gani? Mheshimiwa Waziri, naomba utumie u-profesa wako kwenye hii bandari ili tuone matunda ya degree nne yako wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunamuomba Mheshimiwa Waziri, dunia imeshabadilika, dunia sasa hivi iko kwenye ushirikiano kati ya Serikali na watu binafsi, kati ya Serikali na Serikali na ndiko dunia ilikofikia. Nenda Marekani, Japan kote wanafanya ushirikiano; lakini sisi tuking’ang’ana Serikali kwa sisi wenyewe hatuwezi kufanya, kwa sababu hata tunavyovifanya sisi wenyewe vimetushinda. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Pofesa Mbarawa, tuna Imani kubwa sana na wewe nenda ukalitafakari jambo hili vizuri uone nchi inakwenda kunufaika vipi ili tuweze kupata tija katika taifa letu. Kwa sababu hiyo, Mheshimiwa Waziri uwezo wako tunaufahmu hakika tunajua kwamba jambo hili litakwenda vizuri na tunaomba utulize sana akili ili nchi iweze kunufaika na bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hiyo naunga mkono hoja.