Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Twaha Ally Mpembenwe (21 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuwa mchangiaji wa kihistoria leo kwa kuwa mchangiaji wa kwanza katika session hii ya jioni.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nichukue fursa hii kwanza kabisa kuipongeza Ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa uwasilishaji mzuri. Kwa kweli hotuba hii imetupa dira nzuri ya kuonyesha kama Serikali wapi tulikotoka, nini kimefanyika na yale ambayo tunakusudia kwenda kuyafanya katika kipindi kijacho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo sitakuwa mzungumzaji wa mambo mengi sana, lakini nataka niguse tu katika maeneo kadhaa hasa katika miradi mikubwa ambayo Serikali wameweza kuitekeleza na wanakusudia kuitekeleza. Baada ya hapo, nitagusia kidogo mambo mawili, matatu katika jimbo langu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wazungumzaji wengine kusema kwamba ni ukweli uliokuwa wazi kwamba legacy aliyoiacha Hayati Dkt. John Pombe Magufuli itakuwa inaenda kujieleza yenyewe. Kwa tafsiri hiyohiyo, ni matumaini yangu kuwa tunategemea kuanza kuona legacy mpya ya mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan hasa katika kukamilisha miradi mikubwa ya kimkakati ambayo imeachwa na predecessor wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu niguse miradi ya kimkakati, kwa mfano mradi wa SGR, ni muhimu sana kwani unakwenda kufanya total transformation ya social economic transformation katika nchi yetu. Especially katika maeneo yote yale ambayo yatakuwa yanapitiwa na mradi ule, tunategemea kwa namna moja ama nyingine kutakuwa na mabadiliko makubwa sana ya kijamii na kiuchumi vilevile. Hivyo, ni mategemeo yangu kuona Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan wanakwenda kukamilisha miradi hii. Hii itatuwezesha sisi kama Serikali au kama Taifa kuwa na mapato ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba vilevile nizungumzie mradi mzuri sana wa ndege. Mradi huu wengi sana wamejaribu kuongeaongea na wale rafiki zetu wengine ambao wako form six, walio-graduate kule marafiki zangu, waliweza kuzungumza mengi sana katika mradi huu. Nataka niseme tu mradi huu mama yetu ameanza vizuri sana, alianza kwa salam nzuri ya kuwasalimia Watanzania, kwa kusema nawasalimu Watanzania kwa salaam ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na alisema kazi inaendelea katika majibu hayo. Katika majibu hayo mama ameanza vizuri, tayari yale malipo ya ndege tatu yameshakamilika, hivyo tunategemea kwenda kuona ndege nyingine zinaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirudie tena katika jambo hili la mambo ya ndege. Katika sekta nzima ya mambo ya aviation, sekta hii siku zote tafsiri yake pana ni kwamba inakwenda kuchochea uchumi wa nchi. Tunavyokuwa na National Flag Carrier maana yake ni kwamba tunakwenda kuitangaza nchi. Hivyo basi, niseme tu kama Serikali wamefanya jambo la busara na Mheshimiwa Rais alivyoweza kuzilipa ndege hizi tunakwenda kuona sasa mabadiliko makubwa yanakwenda kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwatoe shaka Wabunge wenzangu, lakini vilevile na Watanzania kwa ujumla, kale ka-hasara kalivyokuwa kamezungumziwa, najaribu ku-refer kule katika Ripoti ya CAG isije sana ikatuumiza vichwa. Wenzetu Kenya mwaka jana waliweza kutengeneza loss ya Dola milioni 338; mwaka 2019 walitengeneza loss ya Dola milioni 258; mwaka 2018 walitengeneza loss ya Dola milioni 100 lakini bado wako stable, tafsiri yake ni kwamba wanafanya vizuri katika sekta tourism.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niweke ufahamu vizuri hapa kwa Watanzania pamoja na wale Wabunge wenzangu ambao ni form six. Tafsiri yake ni kwamba katika accounts kuna kitu kinaitwa net off maana yake ni kwamba kama kuna hasara inapatikana katika sekta moja inakwenda kuwa compensated katika sekta nyingine. Sisi kama Tanzania tumefanya vizuri na maono mapana ya Hayati Dkt. John Pombe Magufuli ni kuhakikisha kwamba tunakwenda kuimarisha suala zima la tourism. Hivyo, naiomba Serikali, twendeni tukapambane ili tuweze kuhakikisha tunakwenda ku-boost internal tourism ili sasa ndege zetu hizi zilizopatikana ziende kufanya vizuri kama kwa neighbor zetu wa Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie mradi wa hydroelectric power. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, alikwenda katika eneo ambapo mradi ule unafanyika, maelezo aliyoyatoa ni ya faraja na ya kuwatia matumaini hasa Watanzania na vilevile wajomba zangu wa Rufiji na sisi watu Kibiti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu unafanyika katika maeneo makubwa mawili, kuna upper stream na downstream. Sisi tupo kule katika maeneo ya downstream, kuna hekari takribani 150,000, napenda sana kuiona Serikali sasa inakwenda kujielekeza katika mradi ule ili sisi watu wa Kibiti na Rufiji tuweze kunufaika katika masuala mazima ya umwagiliaji. Kilimo cha umwagiliaji ni cha msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu unavyokwenda kukamilika na tumeambiwa kwamba fedha zipo na mimi sina shida na sina shaka na Serikali ya Awamu ya Sita najua fedha zipo na mengi yameshaanza kufanyika. Ni imani yangu kwamba tutakwenda kuwa na mradi wa umwagiliaji ili tuweze kuhakikisha mradi huu ya hydroelectric power unakwenda sambamba na mradi na mradi ule wa umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee sasa mambo yangu ya jimboni. Nimshukuru tu Mheshimiwa Rais ameanza vizuri, kama alivyoanza kusema kwamba kazi inaendelea, ni kweli kazi inaendelea. Hivi ninavyoongea tayari shilingi milioni 594 zimeshapelekwa katika kumalizia jengo la Mheshimiwa Mkurugenzi wetu wa Wilaya. Sambamba na hilo tumeweza kupewa fedha takribani shilingi milioni 500 tunakwenda kujenga wodi tatu katika Hospitali ya Wilaya. Tumepewa fedha nyingine shilingi milioni 180 katika kukamilisha maabara 6. Fedha hizi zimepatikana kutokana na mama huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hiyo haitoshi, tumeweza kupewa fedha nyingine takribani shilingi milioni 136 katika mradi wa maji. Hivi navyozungumza tayari katika Kata ya Dimani maji yanatoka, mambo yetu yanakwenda bambam. Nani kama mama?

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, mama huyu ameyafanya mambo mazuri na sisi ni mategemeo yetu anakwenda kuyafanya mazuri zaidi katika kuhakikisha kwamba kauli yake inayosema kazi inaendelea ni kweli kazi inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, haya it’s not a rocket science, ni vitu ambavyo viko wazi, tayari tumeshalipa ndege tatu nani kama mama?

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, imani yangu kubwa Zaidi ni kwamba mama yetu Samia Suluhu Hassan anakwenda kutengeneza legacy nyingine ambayo ameiacha predecessor wake ya kukamilisha miradi mikubwa hii ya SGR na Hydroelectrical power na mingine kama nilivyokuwa nimezungumza. Kama hiyo haitoshi ametuambia Mheshimiwa Ummy Mwalimu hapa tunakwenda vilevile kujenga Vituo vya Afya katika wilaya zile ambazo bado hazijafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima na unyenyekevu wa hali ya juu kabisa, napenda kusema naunga mkono hoja. Tumuombee mama yetu ili aweze kutusogeza mbele. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa, nichukue fursa hii kuipongeza Wizara kwa wasilisho zuri ambalo wameliwasilisha mbele yetu na sasa hivi tunalijadili. Kipekee nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu mkubwa sana aliokuwa nao na ushirikiano ambao anauonesha kwa Wabunge wote ambao tunazungukwa na maeneo haya ya uvuvi.

Mheshimiwa Spika, vilevile nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri. Mheshimiwa Rais alivyoweza kumpa nafasi hii tena kwa kumtoa kwenye sehemu ya michezo, Mheshimiwa Rais alifanya maamuzi yaliyokuwa asilia. Kwa sababu Mheshimiwa Naibu Waziri yeye ni mzoefu na ni institutional memory katika Wizara hii. Ana uzoefu mkubwa sana na ni mtaalam katika sekta hiyo. Kwa hiyo, ni mategemeo yangu kwamba anakwenda kushirikiana na Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalam katika Wizara husika ili kuweza kuleta mabadiliko makubwa zaidi kwa maslahi mapana ya wananchi wa Tanzania na bila kuwasahau watu wa Jimbo lake la Mkuranga pamoja na wajomba zake wa pale Kibiti.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie Wizara hii katika eneo moja tu la uvuvi. Mchango wangu utakuwa umegawanyika sehemu kubwa mbili, sehemu ya kwanza nitachangia kitaifa zaidi lakini sehemu ya pili nitarudi kule katika Jimbo langu la Kibiti pamoja na wajomba zangu wa Mkuranga ambao tuna adha kubwa sana kuhusiana na suala zima la mambo ya kamba.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli ulio wazi kabisa kwamba rasilimali tulizonazo sisi Tanzania katika maeneo yetu ya uvuvi ni rasilimali tosha kabisa kuonesha kwamba pato letu la Taifa linaloweza kuchangiwa na Wizara hii au na sekta hii liwe linakwenda juu siku hadi siku. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake ametuambia kwamba katika GDP tumepata asilimia 1.7 mwaka 2020 na amesema kwamba sekta hii imeongeza uzalishaji imekua kwa asilimia 6. Sasa sielewi tafsiri pana mimi niliyokuwa nayo katika watu wa uchumi tunasema ongezeko hili lime-increase katika decreasing rate.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu mwaka 2013 sekta hii katika suala zima la GDP lilichangia kwa asilimia 2.4, lakini leo tuko mwaka 2020 limechangia kwa asilimia 1.7. Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake ametuambia kwamba kuna ongezeko zuri sana la uzalishaji katika sekta hii, sasa huu uzalishaji ongezeko lake liko very questionable.

Mheshimiwa Spika, Ziwa Victoria sisi tuna asilimia 51, tafiti zilizokuwa zimefanywa na wataalam zinatuambia kwamba tani za samaki zilizokuwa pale ni 3,495,914. Katika Ziwa Tanganyika sisi tuna asilimia 41, tafiti zilizokuwa zimefanywa na wataalam zinatuambia kwamba tani za samaki zilizoko pale tunazungumzia 295,000.

Mheshimiwa Spika, tukienda mbele zaidi kule kwa wakwe zangu katika Ziwa Nyasa sisi tuna asilimia 18.5 katika eneo la uvuvi, tafiti zilizokuwa zimefanywa na wataalam zinatuambia kwamba tani za samaki zilizokuwa pale ni 168,000. Hatujaishia hapo tukienda mbele zaidi kwenye territorial area yetu kule, tafiti zilizokuwa zimefanywa na wataalam tunaambiwa tuna tani 100,000 za samaki. Kule ndani zaidi hatukuweza kufika kwa sababu utafiti bado haujafanyika. In totality tani zote za samaki zilizopo Tanzania tunazungumzia 3,598,914. GDP tunaambiwa kwamba tumechangia kwa asilimia 1.7 hapa kuna shida tena kuna shida ya msingi.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali, Mheshimiwa Waziri ametuambia hapa kuna mambo makubwa ambayo wanakwenda kufanya, mojawapo wanatuambia kwamba kuna meli tunaitegemea itapatikana kwenda kule deep sea. Hii iko very questionable kwa sababu tunachokifanya hapa tunanunua mbeleko wakati bado hata mtoto hajazaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hotuba hii Mheshimiwa Waziri ametuambia kwamba tunakwenda kutengeneza bandari pale Bagamoyo. Sisi ni wageni utatuvumilia vijana wako kwa sababu tunajifunza mambo mengi sana, mwaka 2012 kuna fedha ziliweza kutolewa katika Bunge lako hili karibia milioni 500 za kufanya tafiti jinsi ya kuweza kujenga bandari. Kutokana na taarifa tulizokuwa tumezipitia library huko inasemekana kwamba kule Kilwa Masoko ndiyo bandari ilikuwa inakwenda kujengwa, nini kilichotokea mimi sijui.

Mheshimiwa Spika, leo Mheshimiwa Waziri anatuambia tunakwenda kujenga pale Mbegani safi sana mimi natokea Pwani na nina interest hiyo kwa Pwani lakini na Taifa kwa ujumla wake. Hata hivyo, tunaambiwa kwamba katika bajeti imetengwa shilingi bilioni 50 na sisi tunakwenda na mfumo wa cash budget system pale tunapokuwa tunakusanya ndipo tunapokwenda kutumia, sasa napata shida tunaagiza meli, halafu tunaambiwa tunakwenda kujenga kule Mbegani, tumetenga bilioni 50, where are we going to get the money from? Hapa mimi napata shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ni mhubiri mkubwa sana wa suala zima la PPP. Tukubali, tusikubali Serikali tusiwe tunaingia moja kwa moja kichwa kichwa katika mambo haya. Ni vizuri tukawa tuna-regulate, lakini tunajua kabisa kwamba kuna baadhi ya maeneo katika suala zima la tafsiri ya kiuchumi inaweza ikawa ni controlled economy ikawa mixed economy. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali lazima tuwe tunaangalia jinsi ya kuweza kuingia pale. Ili tuweze kuwekeza jinsi inavyopaswa katika sekta nzima hii ya mambo ya fishery, ni lazima twende katika suala zima la PPP. Mheshimiwa Waziri na wataalam mkae kitako kuishauri Wizara kwamba twendeni kwenye PPP tuwaite watu waweze kwenda kujenga bandari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunavyozungumza kujenga bandari ya uvuvi hiki siyo kitu cha masihara tunazungumza bandari iwe na infrastructure zote zinazoweza kukubalika, ikiwemo suala zima la kutengeneza viwanda, meli inavyokuja inapaki pale, samaki zinaondolewa, kama utumbo unatolewa, watu wanaweka kwenye cold room mambo mengine yanaendelea. Sasa tunakuja kuzungumza kwamba tunakwenda kujenga Mbegani tumetenga shilingi bilioni 50, this is a joke!

SPIKA: Mheshimiwa unayetoka rudi kwenye kiti chako kwa sababu umekatiza kati ya mzungumzaji na mimi. Kwa hiyo, rudi ukae kwenye kiti chako. Nazidi kuwakumbusha kama mzungumzaji anazungumza usikate kati ya mstari wake na Spika. Mheshimiwa Mpembenwe endelea. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, kwa tafsiri hiyo hiyo maana yake ni kwamba sisi ili tuweze ku-move kutoka hapa tulipo kama alivyosema senior wangu pale, kaka yangu Mheshimiwa Mwijage, ni lazima twende katika concept hii ya PPP.

Mheshimiwa Spika, narudia mara kwa mara na nitaendelea kulirudia kwa sababu kubwa moja, sheria ililetwa hapa. Sasa kama hii sheria ilikuwa imekuja kuja tu katika mazingira ya kuja, mimi napata shida. Sheria hii ilikuja hapa na ikafanyiwa amendments, lazima sasa tuweze kutumia sheria hii tuweze kuwaita wawekezaji ili sasa kwa namna moja ama nyingine twende tukajenge bandari na tuweze kuona sekta hii inakwenda kuchangia vile inavyopaswa sio tu asilimia 1.7 twende mbele zaidi. Mheshimiwa Waziri unatuambia kwamba kuna growth ya 6 percent katika production lakini Growth Domestic Product yenyewe imekwenda 1.7 wakati 2013 ilikuwa 2.4, hii ni increase katika decreasing rate, we cannot be able to move in that way. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa tafsiri hiyo hiyo, naomba tena niishauri Serikali, ili tuweze kufanya vizuri zaidi katika eneo hili basi hakuna budi na sisi vilevile katika Wizara hii tutengeneze jeshi letu, kama kule TANAPA mifugo inaibiwa, watu wanachukua kila kitu. Kuna watu wanaitwa DCA, wanachokifanya wao hakuna kitu kingine zaidi ya kutoa tu certificate watu wa Spain au Malabar na meli kubwa kubwa wanatoa tu taarifa tunataka kuja kuvua kule kwenu. Watu wanachokifanya wanaambiwa bwana lipa ada akilipa ada meli inakuja inavua inaondoka. Sasa kuna zile meli nyingine haziwezi zikaja kufunga hapa, hatuna ports ya kuweza kufanya hawa watu waje kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo yako mengi, lakini naomba niende Jimboni kwangu sasa. Jimboni kwangu kuna shida ya msingi sisi tunavua kamba na hapa Tanzania wanavyozungumza suala zima la kuvua kamba wanapatikana pale. Mimi najua baba yangu mzee Mpembenwe siku moja aliwahi kuniambia, yule mnayemuona pale Spika wenu yule aliwahi kuwa Rufiji huku anaijua Rufiji vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme tu kwamba pale Kibiti na Mkuranga sisi tuna shida na Wizara hii, kikubwa wanachokifanya ni kuweka tu mambo ya kitaalam mengi, ma-scientist wanakuwa wengi. Mwaka 2017 wamezuia pale uvuvi wa kamba katika kipindi fulani, hivi ninavyozungumza kamba pale wanavuliwa katika kipindi siyo rafiki. Wakati sisi wananchi wanaomba kuvua kamba katika kipindi cha mwezi Desemba mpaka Mei wao wanatuambia tuanze kuvua kuanzia mwezi Juni kwenda mbele, kipindi hicho wale kamba wanakwenda bahari kuu, wanavyokwenda bahari kuu wananchi wetu hawana vyombo vya kwenda kule. Tafsiri yake ni nini? Tunawaweka wananchi wa Mkuranga na Kibiti katika maisha magumu. Kule ni delta, vile ni visiwa, hatuna zao tunaloweza kuzalisha sisi zaidi ya kamba wale kuweza kutusaidia. Kwa hiyo, hivi vitu lazima tuviangalie kwa upana wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine la kusikitisha zaidi, Mheshimiwa Waziri wiki iliyopita wakati nauliza swali hili Serikalini alisema kwa mapana marefu zaidi, katika kipindi cha miaka mitano mwaka 2015-2020 kamba waliopatikana katika Wilaya ya Mkuranga pamoja na Kibiti ni tani 1,200. Fedha zilizopatikana shilingi bilioni 16 Serikali walipata tozo shilingi milioni 600. Wilaya ya Mkuranga hawakupata senti tano, Wilaya ya Kibiti hatujapata senti tano, sasa mnatusaidia sisi watu wa Kibiti na Mkuranga? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, Wizara lazima iweze kufikiria kutusaidia watu ambao tunaishi katika maisha ya delta, hatuna shughuli nyingine yoyote ya kilimo. Kule mimi niliko nina Kata 5 za Kiongoroni, Mbochi, Mapoloni, Msala na Salale na kule kwa Mheshimiwa Waziri kuna Kata moja ya msingi sana kule…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa kunipa nafasi hii nami kuwa mchangiaji katika hotuba hii ya Mheshimiwa Rais. Naomba tu kidogo nifanye marekebisho hapo jina langu naitwa Twaha Mpembenwe, Seif Mpembenwe alikuwa mzee wangu na tayari ameshatangulia mbele ya haki.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naomba nichukue nafasi hii kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi, wapiga kura wa Jimbo la Kibiti kwa heshima kubwa sana waliyonipa mimi na familia yanguna leo hii niko hapa mjengoni nawashukuru sana. Sambamba na hilo, naomba vilevile nichukue fursa hii kuwashukuru watu muhimu sana katika maisha yangu hasa rafiki yangu mpenzi ambaye ni mke wangu mama Sabrina; wanangu Sabrina, Leyla, Naima na Najma. Nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila nisipoweza kutoa shukrani za dhati kwa aliyekuwa Mkuu wangu wa Wilaya lakini sasa hivi ndiye Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mheshimiwa Joseph Joseph Mkirikiti pamoja na Katibu Tawala wangu wa Mkoa, mama yangu Rehema Madenge wakati nafanyakazi chini yao walikuwa viongozi wazuri na waliweza kuniongoza vizuri na mpaka leo nimekuwa Mbunge katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi watu wa Pwani ni wakarimu sana, halafu tuna desturi ya kuweza kushukuru. Sasa kabla sijaanza kuichangia hotuba ya Mheshimiwa Rais ningependa kuanza kumshukuru Rais Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa mambo makubwa na mazuri aliyoweza kutufanyia watu wa Jimbo la Kibiti.

Mheshimiwa Spika, katika sekta nzima ya afya katika kipindi cha mwaka 2015 - 2020 Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, aliweza kutupatia fedha takriban shilingi 4,021,493,500,fedha hizo ziliweza kutumika katika kuweza kujenga hospitali ya wilaya, vituo viwili vya afya, zahanati tisa na vilevile tumeweza kukarabati kituo chetu cha afya kikongwe cha pale Kibiti. Tunashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika sekta ya elimu,Mheshimiwa Rais aliweza kutupa fedha takriban shilingi 4,243,607,588.99, fedha hizi zimeweza kutumika katika kuweza kujenga vyumba vya madarasa, matundu ya vyoo, nyumba za Walimu na kuweza kukarabati vilevile shule yetu kongwe ya Kibiti Sekondari ambayo ninauhakika kabisa baadhi ya Wabunge hapa wamepita na kuweza kusoma katika shule ile.

Mheshimiwa Spika,kama hivyo haitoshi Mheshimiwa Rais ametufanyia lingine kubwa ameweza vilevile kutupa fedha takriban shilingi bilioni 14.3 katika Kata ya Salale katika Wilaya ya Kibiti pale katika Kijiji cha Nyamisati limejengwa Gati zuri ambalo kwa namna moja ama nyingine limeweza kuturahisishia sisi watu wa Kibiti pamoja na ndugu zetu wa Mafia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hili vilevile naomba ku- declare specialinterest, katika gati lile limeweza kuturahisishia sana sisi watu wa Kibiti kwasababu kule Mafia kuna akinamama kule wa kiarabu arabu na sisi watu wa Kibiti tunakwenda kule kwenda kuoa sasa kuweza kuchanganya mbegu zile. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais katika hilo.

Mheshimiwa Spika, vilevile Mheshimiwa Rais ameweza kutupa fedha takriban shilingi 4,021,850,786.38 fedha hizi zimeweza kutumika katika kuweza majengo ya utawala majengo yale ni mazuri jengo kubwa la Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya na Mkurugenzi Mtendaji, bado kuna fedha kama shilingi milioni 700 tumeweza kuziomba kwa Serikali Kuu ili tuweze kumalizia katika miundombinu masuala mazima ya umeme na maji ili wananchi wale sasa waweze ku-enjoy kuweza kumchagua Mheshimiwa Raisna kuweza kuwa na Mpembenwe kama Mbunge wao.

Mheshimiwa Spika, shukrani hizi bado zinaendelea katika Jimbo letu la Kibiti limegawanyika katika sehemu kubwa mbili kuna sehemu ya geta na sehemu ya juu huku. Katika sehemu ya geta kule Mheshimiwa Rais aliweza kutupa fedha takriban shilingi bilioni 2.5, fedha zile katika kujenga daraja, kuna mambo mambo yaliweza kutokea lakini namshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI ndugu yangu Mheshimiwa Selemani Jafo aliweza kutia mguu, sasa hivi ninavyoongea wakandarasi wako site, mkandarasi aliyekuwa amejenga gati la Nyamisati ndiyo yuko kule shughuli zinaendelea na vijana wetu pale vilevile wameweza kufunguliwa fursa za ajira, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais katika hilo.

Mheshimiwa Spika, kubwa kuliko yote tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweza kuturudishia amani ambayo ilikuwa imepotea katika Jimbo la Kibiti. Jimbo la Kibiti amani ilikuwa ni bidhaa adimu sana. Nataka nieleweshe tu kwamba kuku walikuwa na uhuru mkubwa sana kuliko mwanadamu wa kawaida katika kipindi cha mwaka 2018/2019, lakini Mheshimiwa Rais aliweza kusimama katika nafasi yake kama Amiri Jeshi Mkuu na kuweza kuturudishia amani hiyo. Tunamshukuru sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoa shukrani hizo katika Bunge hili la Kumi na Mbili tumefarijika sana kwasababu tuna kiongozi vilevile wa Chama Cha Mapinduzi naye siyo mwingine ni komredi Humphrey Polepole. Nataka niombe vile vile nichukue nafasi hii dakika moja kuelezea utekelezaji wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi katika Jimbo la Kibiti katika kipindi cha uchaguzi mpaka hivi sasa. Hivi ninavyoongea baada ya kuweza kuwasiliana na wadau mbalimbali nimeweza kufanikiwa kupata fedha shilingi milioni 175 kwa kushirikiana na Mkurugenzi Mtendaji kwa ajili ya kununua ambulance. Fedha hizi zipo sasa hivi katika akaunti ya Mkurugenzi Mtendaji, tukimaliza session hii tu nitamwona Waziri wa Fedha ili tuweze kuweka mustakabali mzima wa masuala ya exemption tuweze kuleta ambulance ile na wananchi wa Kibiti sana waweze kufurahia kuwa na Dkt. John Pombe Joseph Magufuli lakini vilevile kuwa na Mbunge mbunifu ambaye ni Mpembenwe.

Mheshimiwa Spika, kama hivyo haitoshi wakati tukiwa vilevile katika suala zima la kampeni, nilipita huko vichochoroni, nimeweza kuhangaika kwa wadau wangu mbalimbali kwa kushirikiana na Mkurugenzi Mtendaji ninavyoongea tumeweza kupata fedha shilingi milioni 20 kwa ajili ya ujenzi wa dispensary fedha hizo zipo kwa Mkurugenzi Mtendaji wakati wowote kuanzia sasa hivi dispensary ile itajengwa kwa kupitia force account. Hilivilevile linafanyika.

Mheshimiwa Spika, kama hivyo haitoshi vile vile naomba nilitaarifu Bunge lako Tukufu pamoja na kiongozi wetu komredi Humphrey Polepole, madawati 100 tayari yalishasambazwa katika Jimbo la Kibiti na hivi ninavyoongea kuna madawati mengine 500 wiki tatu zijazo yatasambazwa katika shule za msingi vilevile pamoja na shule za Sekondari.

Mheshimiwa Spika, pia naomba tu niseme tutaanza ujenzi wa kituo cha Polisi haraka iwezekanavyo kwa kutumia nguvu zetu za ndani.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa nichangie hotuba ya Mheshimiwa Rais mimi sitaki kwenda mbali nasema machache tu.

SPIKA: Mheshimiwa Twaha sasa hotuba ya Rais sasa. (Kicheko)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sanakatika kuichangia hotuba ya Mheshimiwa Rais mimi nagusa sehemu tatu muhimu. Kwanza katika suala zima la kilimo, najua Wizara ya Kilimo inafanyakazi nzuri sana. Napenda vilevile kumshukuru ndugu yangu Mheshimiwa Bashe kwa hotuba nzuri sana ambayo aliitoa siku alipofanya mkutano kule Tabora you realkneeled down,nilijaribu kumpigia simu lakini hakuweza kupatikana. Nampongeza sana kwa hotuba nzuri na mikakati mizuri ambayo Wizara ya Kilimo sasa hivi wanaendelea.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo kuna shida kubwa sana katika suala zima la bei ya korosho. Bei ya korosho na ufuta kwa wananchi wa Mkoa wa Pwani hususan katika Jimbo la Kibiti imekuwa ni mtihani mkubwa. Sisi tuna watoto wetu wa asili Wamwera, Wamakonde na Wayao kule, wao wanauza kilo moja ya korosho gredi A shilingi 2,700 wakati mwingine, lakini inashangaza sana kuona kwamba baba zao sisi watu wa Kibiti, kilo hizo za korosho gredi A inauzwa shilingi 800. Kwa hiyo naomba niishauri Serikali sasa tuweze kuangalia mustakabali mzima katika kuweza kuangalia minada hiyo wakati inafanyika, ifanyike kwa pamoja kwasababu minada ikiwa inaanza kule kusini halafu baadaye inakuja huku katika Mkoa wa Pwani, inakuwa shida sana, ndiyo wale wanunuzi wanaanza kufanya illegal price fixing, wakati mwingine wanakuja kununua korosho kwa bei ya chini. Mpaka hivi ninavyoongea sasa hivi bado kuna korosho chungu nzima za wananchi wanahangaika nazo kule.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nichangie katika sekta nzima ya mambo ya elimu. Tuna wajukuu zetu hawa sasa hivi wana miaka sita elimu bila malipo imeweza kuonyesha kwamba watoto wengi sana wameweza kusajiliwa kuingia Shule ya Msingi, ikifika mwakani tayari watoto hawa watakuwa wamesha-mature miaka saba imetimia. Kwa tafsiri hiyo tusipokuwa makini elimu bila malipo inaweza ikageuka ikawa timing bomb.

Naomba sasa kuishauri Serikali, tuweze kwa namna moja ama nyingine kuwaongezea nguvu watu wa Halmashauri turudishe baadhi ya makusanyo, vyanzo vya mapato viende kwao, hivi sasa wawe na mpango mkakati wa kuweza kutengeneza vyumba vya madarasa. Tukifanya hivyo tafsiri yake pana ni kwamba tutakuwa na uwezo mkubwa sana wa kuweza kufanikisha watoto hawa kuingia Sekondari na bila ya crisis ya namna yoyote.

Mheshimiwa Spika, lingine ambalo naomba nilichangie ni katika sekta nzima ya masuala ya uvuvi, nashukuru kwa kengele lakini bado dakika zinaendelea. Katika sekta hii ya uvuvi ..

SPIKA:Ahsante sana.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Delta.

SPIKA: Ooh,muda hauko upande wako Mheshimiwa Twaha.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE:Mheshimiwa Spika, nashukuru nanaunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji katika mpango huu. Lakini awali ya yote kwanza naomba nichukue fursa hii kuwapongeza Wabunge wenzangu ambao wameteuliwa katika portfolio mbalimbali nataka niwaahidi tu kwamba sisi tutaendelea kuwapa ushirikiano katika nafasi zao walizonazo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama hivyo haitoshi vile vile nilikuwa naomba nichukue fursa hii kumpongeza sana Waziri wa Fedha kwa uwasilishaji wake mzuri ambao ameweza kuuwasilisha katika suala zima la mpango huu.

Mheshimiwa Spika, lakini kama hivyo vilevile haitoshi nimshukuru mwenyekiti wetu wa kamati ya bajeti kwa vile vile kuweza kuwasilisha na kuweza kutoa maoni mazuri zaidi kuhusiana na suala la mpango huu.

Mheshimiwa Spika, kubwa kuliko lote nimshukuru Mheshimiwa Rais wetu mama yetu mama Samia Suluhu Hassan ameanza vizuri sana kwa kuweza kuwatia matumaini watanzania ambao walikuwa tayari wameshapoteza matumaini na walikuwa na vilio ndani ya nafsi zao. Lakini mama ameanza vizuri sana na naomba tu nipite katika kauli yake niseme wale ambao wanakusudia kumzingua mama basi tutakwenda kuzinguana nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba ni nichangie mpango huu katika maeneo mawili tu. Eneo la kwanza ni suala zima la tax base na eneo la pili ni suala zima la performance of the projects hizi kubwa kubwa ambazo tunaendelea nazo sisi kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika suala zima la kuchangia kwenye tax base kuongeza wigo wa tax base nilikuwa naomba kidogo nitoe ushauri hapa kwa Serikali. Hizi tough decision kuzichukua wakati mwingine kuzichukua zinakuwa ni ngumu lakini they are wealth taken mimi nilikuwa naomba niishauri Serikali tuangalie uwezekano wa ku-reduce cooperate tax rate tukifanya hivyo tafsiri yake ni nini tutakwenda kutengeneza kitu kinachoitwa multiply effects tunapo reduce cooperate tax rate tunawa-encourage cooperate citizen siyo tu wale kutoka nje lakini hata hawa wa local investors wale wenye mitaji iliyokuwa iko ndani sasa watatoka na watakwenda ku-invest maeneo tofauti.

Mheshimiwa Spika, sasa tunakwenda kutengeneza multiply effect kwa kufanya hivyo. Tafsiri yake pana ni kwamba anapokuja mtu aka-invest, mndengereko kama mimi nikawa na hela yangu ya mkopo nikachukuwa, nikaenda ku-invest kwenye kiwanda, ni kwamba nitaajiri watu. Ninavyoajiri watu, kinachofuata maana yake ni kwamba tunakwenda kuongeza wigo wa tax; na wale watu wanaokwenda kuajiriwa pale, tuta-improve their standard of living.

Mheshimiwa Spika, hii ni very basic economics ya form four sijui form five na nafikiri Mheshimiwa Waziri you know better than this. We have to reduce the corporate tax rate, lazima tucheze na fiscal policy ili sasa tuweze kuwa- encourage investors waje waweze ku-invest. Mama yetu alisema hii katika hotuba zake katika mambo aliyokuwa anazungumza, kwamba lazima tutumie fursa mbalimbali ili kuhakikisha kwamba hatuwakumbizi wawekezaji, tunawavuta ili tuendelee kuwa nao. Kwa kufanya hivyo, tafsiri yake ni kwamba lazima tuchukue tough decision. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna nchi ambazo zimeweza kufanya hivyo. Marekani katika miaka ya nyuma huko waliweza ku-reduce tax corporate rate na athari yake ni kwamba, kukawa na viwanda vingi, wawekezaji wakawa wengi waka-increase vilevile rate employment. Tukifanya hivyo, ile corporate tax base tunaiongeza.

Mheshimiwa Spika, wale watu ambao tunawakamua; nakumbuka kuna Mheshimiwa Mbunge mmoja; mwanangu mmoja kutoka Mtama aliwahi kuzungumza kwamba ng’ombe tunamkamua mpaka inafikia hatua sasa hakuna cha kumkamua. Tafsiri yake ni kwamba we do have to expect kwamba hawa larger tax payer ndio watakuwa wao tu peke yao wanaweza waka- finance hizi fedha ambazo tunaenda kuzikusanya kwa ajili ya shughuli mbalimbali za kimaendeleo ndani ya nchi.

Nilikuwa naomba nishauri katika eneo hilo. Eneo la pili katika suala lazima la kungoze hii tax base…

SPIKA: Mheshimiwa Twaha, mwanao anakuangalia.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, mwanangu ananiangalia!

SPIKA: Mh! Endelea Mheshimiwa. (Kicheko)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Sawa. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, vile vile katika suala la kuongeza hii tax base nilikuwa naomba niishauri Serikali tuongeze wigo, tumefanya vizuri sana katika suala zima la electronic stamp, tumefanya vizuri sana kule kwenye wine katika mambo ya spirit tumefanya vizuri sana kwa sababu tumeweza ku- increase ile collection. Kwa mfano tumeweza ku-increase domestic collection 74.4 percent katika quarter ya kwanza ya 2020.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Value Added Tax ilikuwa imeongozeka 22.8 percent, vile vile tumeweza ku- increase suala nzima la makusanyo ya soft drinks kwenye asilimia 11.7. Hapa tumefanya vizuri. Sasa ni muhimu vile vile Serikali tukaongeza ile electronic stamp katika point of production kwenye maeneo mengine. Kwa mfano katika sekta nzima ya uzalishaji wa cement, kule bado hatujakugusa.

Mheshimiwa Spika, watu wengi sana wanatumia cement na action ambayo inafanyika kule, we can not control it. Katika maeneo mazima ya mambo ya nondo, mabati, we cannot control it. Kwa hiyo, ili sasa ili tuweze ku- extend ile tax base, mambo ya namna hii lazima tuweze kuyashungulikia. Tumefanya vizuri, lakini naomba kuishauri Serikali tuendelee kuweka msisitizo katika maeneo hayo mengine ili sasa tusije tu tukawabana wale larger tax payers peke yao. Wanatukimbia, wanaondoka.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana mama yetu wakati anahutubia Taifa, watu wengi sana waliweza kupongeza hotuba ya Mheshimiwa Rais. Wakati nikiwa hapa, Wandengereko wenzangu kutoka Kibiti walikuwa wanapiga simu na kutuma message kedekede wakisema kwamba sasa jembe limekuja na tunakwenda kufanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni lazima tuangalie, hii tax burden tuweze kui- balance. Tukifanya hivyo, nafikiri tutafanya vizuri sana, collections zetu za ndani zinaweza zikaongezeka.

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ambayo nilikuwa naomba niichangie ni katika suala la zima la PPP. Mimi ni mgeni hapa Bungeni, lakini I know for sure, kwa kupitia paper works nilijua kuna Sheria ya PPP ililetwa hapa na ikaja mwaka 2018 kufanyiwa some amendments. Nilikuwa naomba niishauri tena Serikali, kama kuna upungufu katika sheria ile, basi iletwe tena tuweze kuishungulikia, kwa sababu miradi mikubwa mikubwa hii ni lazima tuifanye kwa kupitia PPP. Tukifanya hivyo, tafsiri yake ni kwamba haka kasungura kadogo, fedha zetu hizi za ndani tunazozikusanya zinaweza zikaenda kutusaidia ili kuweza kuendeleza huduma za jamii.

Mheshimiwa Spika, mfano katika Sekta za Afya na katika mambo mengine fedha hizi zinaweza kutumika. Kwa hiyo, miradi mikubwa mikubwa hii ili tuweze kuiendeleza vizuri zaidi, basi ile idea ya PPP tuilete tena hapa kama ile sheria ina upungufu. Kwa sababu tunapozungumzia PPP, tunazungumzia mifano tunayo pale ndiyo, tumejenga mabweni, lakini tuzungumzie substantial, ile miradi mikubwa mikubwa kama Serikali. Tunakwenda kutengeneza pale mradi wa Mwalimu Nyerere. If not, twendeni kwenye PPP. Najua tunatumia fedha zetu za ndani, ni suala la busara zaidi.

Mheshimiwa Spika, kama hivyo haitoshi, siyo vibaya vile vile, tukiona kwamba mazingira siyo rafiki and of course it has to be so, twendeni tukatumie PPP ili sasa kwa namna moja ama nyingine, miradi hii iende sambamba na iweze kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, uliweza kutoa hapa maelezo kidogo kwamba mabehewa siyo lazima tu yashughulikiwe na watu wengine, sisi wengine tuliwahi kupata bahati kukaa kwa Wandengereko nchi za nje huko, tuliona. Ukienda pale UK utakuta zile British reli zinazokuwa zinazunguka, siyo zote zinakuwa controlled na British Government. Unaweza ukakuta kwamba kuna tajiri tu mmoja anashughulikia eneo fulani, tajiri mwingine anashughulikia eneo fulani lakini mambo yanakwenda.

Mheshimiwa Spika, when you talk about infrastructure in UK it is superb, ipo namba moja. Sisi twendeni tukaige mambo haya, wakati ndiyo huu. Mama tunaye, Mheshimiwa Samia anatupa sana uwezo sisi Watendaji. Ameweza kutupa fursa kusema kwamba tumieni vipaji mlivyonavyo ili tuweze ku-extend tax base tuweze kuongeza maendeleo.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba sana nichangie katika haya maeneo mawili. Hata hivyo, katika suala hili la tax base nitakwenda kwa Mheshimiwa Waziri kwa wakati maalum kumpa takwimu ambazo ni research ambayo nimeweza kuifanya kwenye Commercial City pale Dar es Salaam. If you look at the number from 2015 to date, the number of corporate citizen ambazo tayari zimeshafungwa they are so many.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia amount of tax tunazo- collect zina-increase katika decreasing rate, iko pale Dar es Salaam. Mheshimiwa Waziri akiniruhusu, mimi nitakwenda, nitamfuata, nitampa research ambayo tulikuwa tumeifanya. Sasa ni lazima tuchukue maamuzi magumu ili tuweze kusonga mbele na tuweze kum-support mama yetu katika kuweza kuleta maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. Awali ya yote nichukue fursa hii kwanza kabisa kumpongeza ndugu yangu Juma Aweso, Waziri, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya katika WIzara hii. Sambamba na hilo, niseme tu unyenyekevu aliokuwa nao, mabega yake kuwa chini, basi aendelee kuwa hivyo hivyo. Nasema haya kwa sababu japokuwa mimi ni mgeni hapa Bungeni, sijwahi kusikia hata siku moja Mbunge yeyote akisema kwamba Aweso hapatikani kwenye simu, Aweso hana ushirikiano. Hivyo, nampongezahukuru sana Mheshimiwa Aweso kwa kazi yake hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila vile vile, Mheshimiwa Naibu Waziri anafanya kazi nzuri sana. Tangu nifike hapa, kila Mbunge ambaye anamwomba kwenda nae katika Jimbo lake kuzungumza kero za wananchi analifanya hilo. Ni mategemeo yangu vile vile nitamwomba Kiti kikiridhia ili niweze kwenda nae kule Kibiti twende tukazungumze na wananchi wale kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichangia katika Wizara hii jambo moja tu la Kitaifa la msingi. Nalo ni kuweza kuwa na timu maalum katika Kanda hizi ili ziweze kufuatilia miradi mikubwa mikubwa. Tukifanya hivyo, tafsiri yake ni kwamba tutakuwa tunakwenda kurahisha mzigo mkubwa ambao Mheshimiwa Waziri anakuwa nao kila wakati. Yeye atakuwa anapokea zile taarifa, akiwa anakwenda kule tayari ana taarifa in advance. Kwa hiyo, tukifanya hivyo itamsaidia sana Mheshimiwa Waziri katika kuweza kui-control hii miradi mikubwa mikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nizungumze pale Jimboni kwangu. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, katika bajeti ambayo ilikuwa imetengwa mwaka 2020/2021 tuna miradi takriban kama minne. Kuna mradi mmoja uko kule Mtunda takriban shilingi milioni 736, mradi ule mpaka hivi sasa bado haujaanza na fedha bado haijapelekwa. Kuna mradi mwingine uko kule katika Kata ya Mahege, takriban shilingi milioni 402, fedha bado hazijapelekwa nayo ilikuwa ni bajeti ya mwaka 2020/2021. Lakini kama haitoshi, kuna mradi ambao uko katika Kata ya Mjao shilingi milioni 486, bado vile vile fedha hazijapelekwa, nayo ni bajeti ya mwaka uliokuwa umepita.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale anapotoka Mbunge kabisa katika Kata ya Mtawanya, kuna mradi wa shilingi milioni 61. Chonde, chonde Mheshimiwa Waziri, sitaki kuamini akili yangu kwamba fedha hizi hazitokwenda kwa sababu anakujua. Uchapakazi aliokuwanao Waziri, mambo makubwa ambayo anaendelea kuyafanya katika sekta hii, naamini tu kwamba ni kiasi cha kusema muda utafika, fedha hizi zitakwenda. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri tuweze kwenda kufanya taratibu za msingi kupeleka fedha hizi ili sasa miradi ile iweze kwenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri tu kama mambo yatakuwa mazuri ukipata ruhusa kule Tanga. Miradi hii itakapokuwa imekamilika, nataka nimhakikishie Waziri, sisi watu wa Kibiti tuna zawadi tumemwandalia pale. Atakapokuja kama atakuwa
amepata ruhusa kuna zawadi ya mathna tunaweza tukampatia ili sasa kwa namna moja au nyingine mambo mazuri yaendelee kufanyika na wananchi wale waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumze jambo moja la msingi kubwa sana ambalo limewagusa sana watu wa Kibiti pamoja na Wajomba zangu wa Rufiji pale. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba upembuzi yakinifu unaweza ukaenda kufanyika katika Bonde la Mto Rufiji. Nataka nimwambie, hii kauli ni kauli ya matumaini makubwa sana kwa wajomba zangu wa Rufiji na sisi vile vile watu wa Kibiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka Mheshimiwa Waziri, aamini hili, katika Jimbo la Kibiti kuna kata tangu jimbo lile lianzishwe hazijawahi kuwa na bomba. Kuna Kata ya Kiongoroni, kuna Kata ya Mbuchi, kuna Kata ya Maporoni, kuna Kata ya Msala, hizi kata hazijawahi kuona bomba la maji likiwa linafunguliwa. Kwa hiyo, uanzishaji wa mradi ule utakapokuwa umefanikiwa, nimhakikishie Waziri kwamba, tutamwongeza zawadi nyingine. Tutakwenda sasa katika mambo ya wathulatha sio tu mathna.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa heshima na taadhima na unyenyekevu wa hali ya juu sana, naomba niunge mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia katika hotuba hii ya Waziri wetu wa Fedha ambao ni Wizara muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kabla sijaanza kuchangia, nilikuwa namba nichukue fursa hii kwanza kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa utulivu mzuri sana walionao. Lakini cha kusikitisha tu kwa Mheshimiwa Waziri ni pale tu ambapo timu anayoi-support haiendani na utulivu alionao. Nilikuwa naomba tu kama ikiwezekana ajifikirie mara mbili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaendelea mbali kuchangia hii, naomba tu niseme kwamba kutokana na hali ambayo wanayo watani wetu wa jadi na Mheshimiwa Waziri yeye ni mpenzi sana wa timu hiyo, basi nilikuwa namuomba sana Mheshimiwa Waziri afikirie, ikiwezekana lile goli alilokuwa amelifunga kijana wetu Morrison wakati anacheza na timu ya Namungo kule Ruangwa, basi lifanyiwe credit rating ili sasa liweze kuwasaidia jamaa zetu waweze kwenda kukopea katika financial institution waweze kuendeleza timu. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba kuchangia katika Wizara hii kwenye kifungu Na. 50 na kifungu hiki nagusa tu katika ile sehemu ya TRA. Nitachangia kwenye point moja tu na point hii ni suala zima la tax administration. Ni masikitiko makubwa sana kwenye TRA pale Tax Administration yetu haiko vizuri, kuna leakage katika tax system yetu. Hii leakage inasababisha sisi kama Serikali kukosa mapato mengi sana na mfano wake uko wazi kabisa. Sisi badala ya kuchukua solution kwenye kufanya tax administration, tunakwenda kuchukua solution katika kuongeza tax. Hii inaleta shida sana, tunakuwa hatuwasaidii kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, in recent past kulikuwa kuna issue moja inahusiana na masuala mazima ya mafuta ya kupikia/ crude oil kutokana na common market tulikuwa tumekubaliana kwamba itakuwa zero rated. Sisi Tanzania ilikuwa zero rated, lakini katika mazingira ya kutatanisha kutokana na tax administration, kutokana na leakage iliyopo ndani ya mifumo tukajikuta kwamba tunakwenda kutoza asilimia 10. Hii ni kwa sababu kuna baadhi ya wafanyabiashara walikuwa hawako honest enough, wanakuwa wanaleta semi refined wakati huo huo wana- declare kwamba wameleta crude oil.

Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha, pale kuna TRA, TBS, and by then kulikuwa na TFDA. Hawa wote walikuwa wanaidhinisha kwamba hii ni crude oil, lakini in the real sense mle ndani kulikuwa na semi refined. As a result, Serikali tukaona kwamba tunapoteza mapato. Tulifanya nini? Badala ya kuwa na control nzuri katika tax system, tulichokifanya tukaenda kuongeza tena tax, tukasema wataenda kulipa asilimia 25. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa angalia, anayeathirika hapa ni mwananchi na bahati mbaya sana wenzetu kule katika common market ndiyo, Uganda wao wanakwenda katika asilimia 10 lakini jirani zetu Kenya wao ni zero rated crude oil. As a result, viwanda vyetu vilivyokuwa ndani, vinashindwa ku-compete na viwanda ambavyo viko kule Kenya. Sasa hii, athari yake kubwa ni kwamba tunakwenda kuwakandamiza wananchi lakini hatufanyi solution iliyokuwa sahihi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba katika tax administration, Mheshimiwa Waziri uangalie sana kwenye eneo hili ili sasa kwa namna moja ama nyingine tuweze kuona ni jinsi gani zile leakage tunaenda kwenda kuzi-control. Katika tax administration hiyo hiyo naomba vilevile nizungumzie suala zima la electronic stamp system.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge mmoja amelizungumza vizuri na dada yangu Mheshimiwa Halima Mdee naye akaenda kulikazia. Naomba niseme tu hapa tuna shida. Shida iliyopo ni kubwa sana. Katika mfumo ule, nasema uko vizuri zaidi, tunafanya vizuri, katika baadhi ya maeneo tunafanya vizuri lakini bado tunapaswa twende kuongeza katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, shida kubwa ambayo ninaiona pale ni kwamba vendor ambaye kazi yake ni very simple ni ku-scan tu zile chupa halafu at the same time anakwenda kulipa fedha. Kwa mfano, research niliyokuwa nimeifanya pale Cocacola, bottles ambazo zinakwenda kuwa scanned katika msimu wa mwaka jana zilikuwa almost milioni 600 na katika kila chupa moja inakuwa-charged shilingi 900. Hii shilingi 900 haiendi Serikalini, inakwenda kwa vendor. Cha kusikitisha, tunao watu wa TTCL, TCRA wapo na wao ndiyo wataalam katika mambo ya mtandao. Tunaweza vilevile tukawa-equip wao wakaweza kwenda kufanya kazi hiyo ili sasa zile fedha zinazoweza kupatikana zinakuwa zinazunguka ndani. Hii ni shida katika tax administration yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hivyo haitoshi suala lingine la kusikitisha zaidi sisi Wabunge tunaishi sana kwa kupitia wadau hawa. Kwa hiyo, tunapenda sana kuandika andika paper hizi tunakwenda kwa wadau basi wakiangalia pale wanapoweza kwenda kusaidia kwenye masuala mazima ya corporate social responsibility wanafanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilikutwa na mtihani mkubwa sana baada ya kuwa nimeandika paper kwenda sehemu fulani na kule nilikokuwa nimekwenda yule bwana akanipigia simu akasema bwana tunakuhitaji njoo. Nikajua nakwenda nimefanikiwa. NIlipofika pale, nilisikitika; kutokana na taratibu za kanuni zetu naomba tu nihifadhi kampuni hiyo. Nilifika, nilisikitika akaniambia Mheshimiwa Mbunge tungependa kukusaidia, lakini tunadai sisi Serikalini hapa hii tax return inakuwa ni shida upande wetu. Kwa hiyo, hili ni tatizo katika suala zima la tax administration. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki ambacho sisi tunacho hivi sasa, ni muhimu sana Serikali tukaanza kufikiria katika suala zima la tax refund, input and output VAT basi twende tukawarudishie wale corporate citizens ili sasa kwa namna moja ama nyingine waweze kuzizungusha zile hela katika mfumo na mambo yaweze kwenda kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hili ni jambo la msingi sana kwa sababu tunajua kutokana na masuala mazima ya Covid, crisis za kiuchumi ambazo zimejitokeza in recent past, sisi kama Serikali hatuna budi. Najua tunao uwezo wa kuweza kutumbukiza stimulus package lakini kabla hatujafika huko basi hivi vidogo ambavyo tunaweza tukavifanya katika tax administration twende turudishe fedha zile ile fedha zile zirudi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha kusikitisha katika kampuni moja tayari kuna watu wameshafanywa kuwa redundant almost 600 peoples, watu hawa Serikali tunakosa tax. Hii inasikitisha sana. Kwa hiyo, nilikuwa naomba nisisitize kwa Mheshimiwa Waziri aweze kuliangalia hili kwa mapana yake ili sasa kuweza kuona tunakwenda kuweka internal control nzuri katika suala zima la tax administration. Sio tu tunaongeza tax, lakini tujue kwamba tunavyokwenda kuongeza tax, wanaokuwa wanaathirika ni wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiwa hapo hapo katika suala zima la tax administration, napata shida kidogo katika suala zima la ku-quantify vile vigezo katika Jimbo moja au Wilaya moja na Wilaya nyingine jinsi ya kuweza ku-meet target ya kuweza kukusanya.

Mheshimiwa Spika, pale kwangu Kibiti, nina shida, najua tunafanya kazi vizuri, tunashirikiana karibu zaidi na watu wa TRA, lakini wakati mwingine inakuwa ni husstle kwa wananchi hasa ninavyoona mama zangu wale, mama ntilie wanakwenda kuwa chased out ili kuanza kwenda kulipia kodi. Hii ni shida ya msingi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana Mheshimiwa Waziri tuweze kuliangalia hili ili sasa tuweze kuona vigezo vile ambavyo vinasababisha kuweza ku-meet target katika Jimbo au katika Wilaya moja na wilaya nyingine. Hili ni suala la msingi na haya yote yapo katika suala zima la tax administration. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, hapa hapa katika suala zima la tax administration ni ukweli ambao ulikuwa wazi huwezi kuingia peponi lazima ufe kwanza na ukifa hakuna atakayethibitisha kama unakwenda peponi au unakwenda motoni. Hatuwezi sisi kukusanya kama hatuwezi ku-spend. Lazima tuweze ku-employ enough people ili sasa tuweze kuona wanakwenda kutusaidia katika kuweza kufanya collection. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pale kwangu Kibiti tuna watumishi watatu wa TRA mbaya zaidi watumishi hao watatu wanahudumia vilevile Wilaya ya Rufiji. Sasa hapa mimi napata shida yaani ili tuweze ku-enjoy huwezi ukaenda peponi u-test kwanza kifo, toa fedha ajiri watu. Watu hao utakaoenda kuwaajiri ndiyo watakaoweza kwenda kukufanyia kazi ya kukusanya mapato. Kwa hiyo, nashauri sana hilo lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tu nirudi kwa Mheshimiwa Mbunge mwenzangu wa kule Ujiji. Yeye aliuliza, je, ni busara na mimi nauliza hivi ni busara kweli wilaya mbili zinahudumiwa na wafanyakazi watatu wa TRA halafu tunategemea tuwe na efficiency? We can not be able to move in this way. Kwa hiyo, naomba sana suala hili Mheshimiwa Waziri aweze kuliangalia kwa mapana yake ili sasa tuweze kuona kwa namna moja ama nyingine tunakwenda kuongeza mapato.

SPIKA: Kwa hiyo, Mheshimiwa Mpembenwe kwa kila Wilaya moja mtumishi mmoja na nusu?

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, hiyo ndiyo hali halisi, halafu tunategemea tuwe na efficiency katika maeneo hayo, hii ni shida kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri anapokuja kufanya hitimisho lake basi tuweze kuangalia ni jinsi gani atakavyoweza kuajiri wafanyakazi waweze kwenda kutukusanyia kodi. Nasi tuweze kwenda kuzungumza kule kwa wananchi kodi zinazokusanywa zinakwenda kutumika katika mambo ya shule, TARURA na sehemu nyingine. Kelele hizi tunazozipiga sisi Waheshimiwa Wabunge TRA wasipoweza kufanya kazi nzuri ya kukusanya mapato hatuwezi tukafanikiwa kwa namna moja ama nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la msingi zaidi ambalo naomba nilisisitize ni hapohapo kwenye suala zima la tax administration…

SPIKA: Haya, malizia basi nakupa dakika mbili.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi narudi pale kwa Mheshimiwa Mbunge mwenzangu asubuhi alivyokuwa ameanza kuzungumzia suala zima la mambo ya interest rate. Hapa kuna tatizo kubwa sana la msingi na katika kifungu namba 50 vilevile central bank wanahusika. Why can’t we do our borrowing ikawa cheaper ili sasa tuweze kurahisisha maisha kwa watu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kinachotokea borrowing is very expensive kwa wananchi wa kawaida, lakini vilevile kwa corporate citizen. Sasa hili jambo Mheshimiwa Waziri kaa na wataalam wako tuweze kuangalia jinsi gani tutakavyoweza kucheza na fiscal policy zetu, borrowing yetu ikawa cheaper ili sasa tuweze ku-stimulate uchumi wa ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima na unyenyekevu wa hali ya juu naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili kuweza kuchangia bajeti hii, bajeti ya kihistoria kabisa. Kabla sijaanza kuichangia bajeti hii nilikuwa naomba tu kwanza nimtoe shaka Mheshimiwa Waziri na kumpongeza yeye pamoja na timu yake. Siku ya tarehe 10 Juni, 2021, wakati ana windup bajeti alisema bajeti hii inaweza kumfanya yeye awe very unpopular Finance Minister kwa sababu yupo tayari kupendwa tu na washabiki wa Yanga na wale Wapiga Kura wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimtoe wasiwasi, nimwambie tu bajeti hii imekufanya kuwa very popular Finance Minister, kwa sababu amekwenda kugusa maisha halisi ya wananchi na amekwenda kujibu maswali ambayo wananchi walikuwa wanahitaji. Kwa tafsiri hiyo hiyo, maana yake ni nini? Amekuwa very popular kuliko alivyokuwa popular kuwa mshabiki wa timu ya Yanga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee kwa kusema kwamba, naomba sasa nichukue nafasi hii, nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa mambo makubwa na mazuri ambayo ameanza kuyafanya tangu alivyoweza kuingia madarakani. Kabla sijaichangia bajeti hii nataka niguse matatu, manne tu ambayo Mheshimiwa Rais ameweza kuyafanya yameweza kutupa matumaini na vile vile kuwapa ladha nzuri sana wananchi kujua kwamba sasa tunakwenda katika kazi yenye kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja la msingi ambalo Mheshimiwa Rais ambalo ameweza kufanya ameweza kutupa fedha za takriban shilingi bilioni 172, zimekwenda katika majimbo ya Wabunge wote ambao wapo ndani humu katika Bunge hili. Ikiwemo kule Mtwara Kusini pamoja na Nkasi vile vile zimekwenda katika maeneo ya Tarime na maeneo mengine. Tumepewa fedha hizo ili kwenda kusaidia katika masuala mazima ya TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hilo halitoshi, Mheshimiwa Rais jambo lingine la msingi ambalo ameweza kulifanya; ameweza kuweka jiwe la msingi katika kuhakikisha kwamba barabara ile Standard Gauge inaanza kujengwa kuanzia Mwanza kwenda kule Isaka na bilioni 300 tayari zimeshatoka. Nani Kama mama? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivyo haitoshi, Mheshimiwa Rais katika jambo lingine la msingi ambalo ameweza kutufanyia sisi Wabunge, ametupa heshima kubwa sana kwani ameweza kuhakikisha kwamba kila Mbunge ambaye yupo ndani humu katika Jimbo lake imechaguliwa kata moja kwenda kujengwa shule ya sekondari. Nani kama mama? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema haya machache, naomba sasa nijikite katika bajeti ambayo bajeti hii imekwenda kutengeneza taswira nzima na kujibu maswali ambayo wananchi wetu wengi sana walikuwa wanajiuliza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja la msingi ambalo limeweza kufanyika katika bajeti hii ni suala zima la kuweza ku-reduce ile tax ambayo wanaenda kukatwa wale wafanyakazi wetu. Imetoka kwenye asilimia tisa sasa inakwenda kwenye asilimia nane. Mheshimiwa Waziri wa fedha naomba tu nimwambie, yuko very popular kwa sababu alichokifanya amekwenda kuwafanya wafanyakazi waendelee kuwa na disposable income ambayo inakwenda kuwasaidia kwa namna moja ama nyingine waendeane na kasi ya kimaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivyo haitoshi, jambo lingine la msingi ambalo limefanyika katika bajeti hii na hili ni la msingi kweli kweli. Naomba tu niseme kwamba kuna katozo kameweza kutozwa kale kanachohusiana na mambo mazima ya mafuta Sh.100. Naomba niseme tu fedha hii ambayo inatozwa ni fedha ya msingi kwa sababu inakwenda kutatua kero za wananchi kule vijijini. Kwa kusema hivyo tafsiri yake ni kwamba, naomba niungane na Mheshimiwa Juliana Shonza yale aliyokuwa ameyasema, akinamama walikuwa wanapata adha kubwa sana. Mazao yetu yalikuwa hayawezi yakaenda katika masoko kwa wakati. Mheshimiwa Waziri, katika jambo la msingi ambalo ameweza kulifanya, hili ni mojawapo. Tunamshukuru sana na tunampongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, katika jambo la msingi ambalo ameweza kulifanya, hili ni mojawapo. Tunamshukuru sana na tunampongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nami niseme tu, bajeti hii tunapoenda kuiunga mkono mpaka wale rafiki zetu ambao tumewafunga speed governor watakwenda kuunga mkono bajeti hii, kwa sababu ni bajeti ambayo kwa namna moja ama nyingine imekwenda kugusa maisha ya wananchi kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo yote, naomba tu niseme TARURA ni sehemu ambayo ilikuwa ina kero kubwa sana. Wakati tunachangia hapa Bajeti ya Wizara ya Ujenzi, kwa mara ya kwanza niliweza kupokea shikamoo ya Mheshimiwa Waziri wakati anataka tuipitishe bajeti ile. Mambo yalikuwa magumu sana humu ndani. Mheshimiwa Rais ameliona hilo. Fedha zinaoenda kupatikana takribani shilingi bilioni 332, tunaweza kuziongeza kule. Hizo tunaenda kuongeza na shilingi bilioni 172 ambazo Mheshimiwa Rais tayari ameshatupa. Haya ni mambo ya msingi kabisa. Nani kama mama? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee mbele. Katika mambo mengine mazuri ambayo bajeti hii imeenda kugusa wananchi, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, wewe utaendelea kuwa popular, ondoka kule katika Yanga, njoo Simba. Moja la msingi umeweza kulifanya, umekwenda kuwasaidia wananchi wanyonge, bajeti imekwenda kuongezeka shilingi bilioni 500 sasa, tunakwenda kutoa mikopo kwa wanafunzi. Nani kama mama? (Kicheko/Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niendelee kusema tu, kule kwangu katika maeneo ya Kibiti na maeneo ya kule Mbeya na maeneo mengine yote, kuna wanafunzi wengi sana ambao wapo katika maisha ya kawaida sana. Bajeti hii imekwenda kuongeza shilingi bilioni 500, sasa wanafunzi wanakwenda kukopa na wanakwenda vyuoni. Nani kama mama? (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niendelee mbele. Mama huyu mambo makubwa sana ameyafanya. Naomba tu niweke rekodi sawa sawa kwenye Hansard, ninaposema mama, nakusudia Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Amiri Jeshi Mkuu, mama yetu Mheshimiwa Nama Samia Suluhu Hassan. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na yote haya, naomba niishauri Serikali katika jambo moja la msingi, hasa katika suala zima la kukusanya mapato. Tozo tulizokuwa tumetoza, shilingi moja, bado haitoshi kwa sababu TARURA mtandao wa barabara waliokuwa nao ni sawasawa na kilometa 108,449.19. Fedha ambazo tulikuwa tumewapa mwaka jana, 2020 zilikuwa ni shilingi bilioni 245. Ili TARURA waweze kufanya kazi kwa usahihi wanahitaji shilingi trilioni moja ili sasa kwa namna moja ama nyingine waende kutatua kero zote. Naomba nitoe ushauri kwa Serikali kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwezekana tuangalie suala zima la TV License. Hili jambo liko wazi. Mimi nilipata bahati ya kwenda kutembea kwa Wandengereko kule. Wao walichokuwa wanakifanya, kuna kitu kinaitwa TV License pale Uingereza. Nasi siyo vibaya tukifanya hivyo. Ukienda katika database ya Azam utakuta watu waliopo. Tuna Azam, Zuku, DSTV, Star TV; in totality, Mheshimiwa Waziri chukua tu kwamba viwers wako 1,000,000, ambao wana-own TV. Wanapokwenda ku-subscribe pale, sisi tuchaji shilingi 1,000 tu kwa kila mwezi. Tafsiri yake ni nini? Tunakwenda kukusanya shilingi bilioni 120. Tukifanya hivyo, tunakwenda kuupanua wigo huu ili sasa tuweze kumsaidia mama, twende tusonge mbele ili sasa hii bajeti ambayo inakwenda kujibu maswali ya wananchi, iweze kukamilika na wananchi hawa wafurahie kuwa na Mama Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kama Amiri Jeshi Mkuu wa nchi yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hivyo haitoshi, eneo lingine ambalo naomba nilikazie vizuri ni katika suala zima la kufanya projects hizi kubwa kubwa. Mnajua tumefanya utaratibu. Mheshimiwa Waziri amekuja hapa, ana taswira nzuri sana ya kusema kwamba tunakwenda kuitengeneza miradi mikubwa mikubwa kwa kupitia mambo mengine kama vile infrastructure bond. Nina ombi vile vile Serikali tuweze kuangalia suala zima la PPP. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, PPP tunapaswa tuitumie kwa namna moja ama nyingine. Siyo vyema kweli kuitumia katika infrastructure kwa sababu najua hilo ni eneo liko very sensitive, lakini tunayo miradi mingine. Kwa mfano, tuna mradi ambao tunakusudia katika Wizara yetu hii ya Uvuvi kwenda kule katika deep sea kuvua samaki. Tunakusudia vile vile kwenda kujenga bandari. Haya hatuwezi kuyafanya kama hatuwezi kwenda katika suala zima la PPP. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, muda huu hautoshi, lakini kule kwetu sisi Wandengereko huwa tunasema, mtu akifanya vizuri sana, huwa tuna ngoma ya kuicheza. Tuna ngoma inaitwa Kinyantindili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiniruhusu nicheze tu kidogo nidemke. Kama utaniruhusu ili tuweze kumpongeza mama. Unaniruhusu? (Makofi/Kicheko)

NAIBU SPIKA: Hapana Mheshimiwa Twaha. Hapana, ahsante sana. (Makofi/Kicheko)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, kama huniruhusu basi mimi nitakachokifanya niseme tu nitakwenda kuandika paper na hii tutaiita concept note. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mama yangu, nakushukuru. Naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Kicheko/Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. Lakini awali ya yote kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa hili kwenye sekta hii na sekta nyingine zote. Dunia inajua, Afrika inatambua na Watanzania tunajua hilo, kwamba Mheshimiwa Rais anafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nichukue fursa hii vile vile kumpongeza Mheshimiwa Waziri, yeye pamoja na Naibu Mawaziri wake waendelee kuwa wanyenyekevu hivi hivi na mabega yao yaendelee kuwa chini. Tunashukuru sana kwa ushirikiano mzuri ambao mnaendelea kuutoa kwa Wabunge wote ambao tuko ndani humu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila, nimpongeze sana Mkurugenzi Mtendaji wa TASAC kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya. Tunahitaji vijana wa namna hii wenye uwezo mkubwa wa kuweza kuleta mawazo yaliyo chanya katika kuweza kuibadilisha nchi hii. Lakini vilevile nimpongeze Mkurugenzi wa TPA, anafanya kazi nzuri sana yeye pamoja na wasaidizi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilikuwa jimboni tunakimbiza Mwenge wa Uhuru. Wakati nikiwa jimboni tulifika katika kata moja inaitwa Kata ya Mahege. Pale watu wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa walikuwa wanapata chakula, lakini nilikuta pale mkutano nimeandaliwa akiwepo Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, mzee wangu alikuwepo pale pamoja na Katibu Mzee wangu Mketo walikuwa wako pale, na wananchi wamejumuika kwa pamoja. Lengo la mkutano ule walimuhitaji Mwenyekiti wa Chama, Mbunge pamoja na Katibu.

Mimi niseme tu nimshumuru sana Mwenyekiti wangu wa Chama cha Mapinduzi Wilaya, Comrade Juma Kassim Ndaluke kwa hekima kubwa aliyo nayo yeye pamoja na Katibu wangu Zacharia na Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya alikuwepo pale. Lengo kubwa la mkutano ule wananchi wale walikuwenda kuniuliza swali moja; hivi Mbunge, kuongea unaongea hivi hata unashindwa kuruka sarakasi na wewe upate barabara hii ya Bungu – Nyamisati? Mbona wenzio wanaruka sarakasi wanafanikiwa wewe una shida gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme tu, nimshukuru sana Mwenyekiti wangu wa Chama Wilaya alitumia hekima kukimaliza kikao kile kwa muda mfupi sana. Aliwaambia wananchi wale pamoja na Katibu wa Chama na Mwenyekiti wake, kwamba yeye ndiye msimamizi wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi Wilaya ya Kibiti. Kwa tafsiri hiyo aliniagiza kwamba Mbunge umekimbiza mwenge leo, lakini nakusamehe usikae kwenye mkesha huu nakuomba nenda Bungeni, tunajua kuna bajeti inaendelea kule ya Wizara hii, kwa hiyo, nenda kalisemee hili kwa msisitizo wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwambie Mheshimiwa Waziri, Bungu – Nyamisati kimekuwa ni kilio cha muda mrefu sana. Sawa mimi utaalamu wa kuruka sarakasi sina basi hata haya ninayozungumza Profesa Mbarawa huyaelewi? Sasa nizungumze lugha gani ili niweze kueleweka? Maana nikizungumza Kindengereko huwezi kufahamu, mimi siwezi kuruka sarakasi, ninachoweza kufanya nicheze ngoma ya kwetu kinyafumbili labda unaweza ukanielewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna shida kubwa sana katika barabara ile, kuna vifo vinatokea. Nataka niseme tu Mbunge mwenzangu wa Jimbo la Mafia ambaye ni Waziri vilevile, juzi saa 10.00 usiku alinipigia simu akiniambia Mpembenwe kuna shida katika ile barabara, kuna lori limekaa vibaya pale, kwa hiyo, wananchi wanapata tabu na mvua ilikuwa inanyesha. Haya ni matatizo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba tu lichukuliwe jambo hili on a serious note. Wananchi wa Jimbo la Kibiti tunahitaji barabara hii, kwa sababu hizi habari za upembuzi yakinifu, usanifu wa kina tumechoka. Wazee wale watakwenda kunihukumu. Yuko pale ndugu yangu Mketo, Katibu wa chama, ni mkorofi kweli kweli, lakini wananchi wa pale nao ni shida moja kwa moja. Mimi pamoja na wananchi wangu tunaomba tusaidiwe katika jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, naomba nizungumze jambo moja la msingi katika Wizara hii na huu utakuwa ni mchango wangu mmoja tu. Naomba nizungumze kuhusiana na suala zima la Bandari yetu ya hapa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Singapore ilipata uhuru mwaka 1965, lakini katika miaka 50 ya nyuma ambayo imepita capital income ya Singapore ilikuwa chini ya dola 324. Mwaka 1975 Singapore per capita income ikawa imebadilika, tunazungumzia dola 60,000 nendeni mkaangalie kule mtapata taarifa hizo. Nini maana yake? Maana yake ni kwamba strategically wameweza kuitumia bandari vizuri ili kuhakikisha kwamba inakwenda kuchangia vizuri kwenye pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana, Mheshimiwa Rais amezungumza katika nyakati tofauti katika hafla tofauti za Kiserikali akiwa anaonesha hisia zake za hali ya juu za kutoridhishwa kwake na jinsi gani performance ya bandari yetu inavyoshindwa kuchangia ipasavyo katika pato letu la Taifa. Niombe, sheria tumezitunga sisi wenyewe hapa na sisi wenyewe ndio tumezipitisha sheria hizi, hivi suala hili la PPP lina shida gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemfuatilia vizuri sana Mheshimiwa Profesa Mbarawa katika hotuba yake, wametenga hela bilioni 88 katika kuweza kufanya kuboresha pale, this is a joke, bilioni 88 haiwezi ikatuambia kitu chochote. Asilimia 46 ndio pekee inapatikana kutoka katika mapato yetu ya makusanyo ya TRA pale bandarini, kwenye mipaka yetu na maeneo mengine. Tunataka kuiona sasa bandari inatoka katika hatua moja inakwenda kwenye hatua nyingine. Nami niseme tu, tumefanya jaribio hilo, pale Tanga kuna fedha zimetumika na Serikali tumeweza kupanua Bandari ya Tanga kwa namna moja ama nyingine. Kwa tafsiri hiyo maana yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumetoka sasa katika metric tones 750,000 tunakimbilia metric tones 3,000,000. Haya yanaweza kufanyika kwenye bandari yetu ya Dar es Salaam. Katika hotuba Mheshimiwa Waziri ametuambia tonnage zilizokuwa zinapita pale ni milioni 20, bado hazitoshi Mheshimiwa Profesa Mbarawa. Naamini, sisi Waswahili tumezoea kusema mzigo mzito mkabidhi Mnyamwezi, lakini naamini hata Wapemba vilevile mzigo mzito wanaumudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Profesa Mbarawa aje hapa na mpango mkakati wa kuweza kuangalia suala zima la PPP tuweze kuwekeza ili sasa tuweze kuona tunakwenda kutatua kero za wananchi kule katika majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wote wamesimama hapa wanazungumza suala la barabara. Wabunge wamesimama katika Wizara zilizopita wanazungumza masuala ya dawa, vituo vya afya na mambo mengine; fedha iko pale bandarini kwa hiyo, tuchangamke tuweze kuhakikisha tunaleta utaratibu uliokuwa sahihi ili sasa tuweze kuona wanakuja hapa wawekezaji wanakwenda kuwekeza pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kitu kimoja; juzi niliweza kuwasiliana na Mwalimu wangu, Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo, aliniuliza hivi Mheshimiwa Mpembenwe una nini la kusema kuhusiana na suala zima la bandari pale? Nikamwambia mimi naangalia katika eneo moja tu, katika economic perspective. Akaniambia hapana, mbali ya economic perspective angalia vilevile suala zima la mambo ya operation, pale pana shida, halafu angalia vilevile suala zima la ownership. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la operation ametoka kuongea hapa ndugu yangu Mheshimiwa Kilumbe; amesema kwamba, pamoja na matatizo yote ya TICTS, lakini fedha walizokuwa wanatoa ni nyingi kuliko zilizokuwa zinapatikana kwa kupitia Mamlaka yetu ya Bandari. Kwa hiyo, niwaombe sana, Serikali waje na mpango mkakati wasiogope, sisi ndio tumetunga sheria. Kama leo Profesa anasimama hapa anatuambia barabara hii inajengwa kwa EC + whatever F, barabara hii inajengwa, why can’t we do this pale bandarini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijana tuliowapata sasa hivi Mkurugenzi Mtendaji anafanya kazi vizuri pamoja na wasaidizi wake. Twendeni tuwape moyo vijana hawa. Hizi ndio brain tunazohihitaji katika nchi hii ili tuweze kuibadilisha. Tusikae na yale mawazo ya kizamani eti tunakwenda kuuza nchi, nchi itauzwa na Mtanzania mwenyewe? Hiki kitu hakiwezekani. Kwa hiyo, niwaombe waje na mpango mkakati, ili sasa tuweze kuona bandari yetu ile inakwenda kuchangia pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, life expectance ya pale Singapore ya watu kuishi unazungumzia miaka 83, kwa nini? Watu wanakula bata. Bandari inatengeneza fedha za kutosha, wananchi wana- enjoy maisha. Hatuzungumzii economic growth isipokuwa tunazungumzia economic development, ndio maana life expectance ya wananchi wa Singapore ni miaka 83. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mtanzania wa kawaida atahangaika hangaika, akishamaliza miaka 60, 60 au 62 akisha- retire tunachukua kamba tatu, safari imeisha. Nini? Ni kwa sababu uchumi wetu unakua, lakini kukua kwake sio uchumi endelevu. Tunapozungumzia economic growth kuna tofauti kubwa sana na economic development. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Profesa Mbarawa ajitahidi na wataalam wake, waje na mpango mkakati tuweze kuhakikisha tunakwenda kuboresha bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bajeti yetu hii na Hali nzima ya Uchumi wa Nchi. Kabla sijaanza kuchangia bajeti hii naomba kwanza nichukue fursa hii kwa heshima, taadhima na unyenyekevu wa hali ya juu kabisa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa hili ili kuleta maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaenda moja kwa moja katika kuchangia bajeti hii, naomba nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa hili. Sambamba na hili kabla sijachangia bajeti hii sina budi kuzungumza yale mazuri ambayo Mheshimiwa Rais ameweza kuyafanya mpaka hivi sasa na hasa nataka nizungumze miradi mikubwa mikubwa.

Mheshimiwa Spika, katika miradi mikubwa mikubwa ambayo Mheshimiwa Rais aliweza kuirithi kutoka kwa predecessor wake tunazungumzia Mradi wa Rufiji Hydroelectric Power, mradi ule fedha zipo, mkandarasi yupo site na shughuli zinaendelea. Sambamba na hilo, kuna Mradi ule wa SGR Dar es Salaam – Morogoro pamekamilika, Morogoro – Dodoma pako vizuri, Dodoma – Makutupora kwenda Tabora, Mheshimiwa Rais tayari ameshaini mkataba wa trilioni 4.41 na hivi ninavyozungumza shughuli zinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sio hivyo tu, katika barabara kubwa kubwa zile na madaraja Mheshimiwa Rais ameweza ku-sign off certificate ya mwisho na kumlipa mkandarasi na amefungua Daraja la Tanzania pale Jijini Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, sio hivyo tu lakini marafiki zangu, wajomba zangu kule Wasukuma pale Busisi -Kigongo daraja lile linaendelea kujengwa na shughuli zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais amekwenda mbali zaidi, katika suala zima la usafirishaji wa anga, tayari amesaini mkataba wa kununua ndege tano zikiwemo mbili zile kubwa kubwa na mambo mazuri yanaendelea.

Mheshimiwa Spika, niliona ni vema kuyazungumza haya kwa sababu Mheshimiwa Rais ameweza ku-prove doubt as wrong, kuna wengi walikuwa na wasiwasi kwamba itakuwa vipi, lakini kwa kufanya hivyo tu, Mheshimiwa Rais amekwenda mbali zaidi, ameanzisha miradi yeye mwenyewe ambayo miradi hiyo historia yake ni ya ajabu sana, niseme tu katika moja kubwa ambalo Mheshimiwa Rais amelifanya ni kusaini mkataba wa LNG trilioni 70, fedha ambazo kwa namna moja au nyingine ni historia ambayo itaendelea kukumbukwa ndani ya Taifa hili. Nani kama Mama Samia?

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee mbele. Naomba sasa nijikite katika bajeti hii. Bajeti hii malengo yake makubwa ni matatu. Lengo la kwanza ni kuweza kufufua uchumi; lakini lengo la pili ni kuboresha sekta za uzalishaji na lengo lingine ni kuhakikisha kwamba bajeti inakwenda kusaidia kasi ya maisha.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli ulio wazi kabisa, hakuna ambaye anapinga, dunia imekumbwa na msukosuko mkubwa katika suala zima la mambo ya kiuchumi, tukianza na suala zima la corona na vile vile katika vita vinavyoendelea hivi sasa. Kwa tafsiri hiyo maana yake ni nini? Ni kwamba gharama za maisha zimekuwa kubwa sana duniani sio Tanzania tu. Bajeti hii naomba niseme tu, Mheshimiwa Mwigulu Lameck Nchemba, inamfanya awe very popular Finance Minister japokuwa mwenyewe huwa anasema kwamba hii bajeti inamfanya asiwe popular Finance Minister. Kwa tafsiri hiyo maana yake ni nini? Imemfanya kuwa very popular Finance Minister kuliko kumchukua mtendaji fulani akampeleka katika timu fulani ambayo haipo hata katika kumi bora Barani Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee mbele, bajeti hii imekwenda kugusa maeneo makubwa mawili; katika level ya kwanza kwenye level ya micro economy na level ya pili katika micro economy Kitaifa zaidi. Ninapozungumza katika eneo la micro economy, bajeti hii ni bajeti ya wananchi kweli kweli kwa sababu: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ameweza kuongeza mishahara kwa watumishi na sasa hivi tunakwenda kuzungumzia asilimia 23. Hili ni jambo la msingi sana. Tunajua gharama za maisha zimeongezeka, kwa tafsiri hiyo hiyo ni lazima vile vile tuweze ku-mitigate na mambo mazima ya mshahara na hilo limefanyika katika bajeti hii. Hongera sana kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, bajeti hii vile vile imekwenda kugusa wananchi wa kawaida sana, nini maana yake? Hivi tunavyozungumza wanafunzi wanakwenda kusoma bure form five and six. Hii inatuambia kwamba, sasa sisi Watanzania kwa raha zetu. Kazi yetu ukipata mtoto, hangaika naye kulea mpaka miaka saba, akitoka hapo darasa la kwanza mpaka la saba bure. Akitoka hapo form one mpaka form four bure. Akitoka hapo form five mpaka form six bure. Akitoka hapo kwenda Chuo Kikuu kuna fedha bilioni mia tano na sabini Mheshimiwa Rais ameziweka zinasubiri vijana kwenda kuchukua mikopo, nini maana yake? Maana yake ni kwamba, wanafunzi kutoka Mbeya, wanafunzi kutoka Songwe, wanafunzi kutoka Handeni, wanafunzi kutoka Kibiti, wanafunzi kutoka Mtama kwa Wamakonde kule, wote wanakwenda Chuo Kikuu bila shida yoyote nani kama Mama Samia. (Makofi)

WABUNGE FULANI: Hakuna.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, naomba niendelee mbele, bajeti hii katika mambo mengine makubwa na mazuri ambayo imeweza kuyafanya imekwenda vilevile kugusa katika ngazi ile ya micro Kitaifa zaidi. Tafsiri hiyo maana yake ni nini, Mheshimiwa Rais amekwenda mbali zaidi, katika Sekta nzima ya Kilimo na inajulikana wazi kabisa Tanzania asilimia 65 tunategemea kilimo. Pale Mheshimiwa Rais amekwenda kutumbukiza fedha takribani shilingi bilioni 954, nani kama Mama Samia. Kwa kufanya hivyo tafsiri yake ni nini, tunakwenda sasa kuboresha sekta nzima ya mambo ya uzalishaji. Kwani tunajua kule kwenye kilimo ndipo tutakapokwenda kupata malighafi ambazo zitakwenda kusaidia kuzalisha products nyingine zikiwepo vilevile za mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Rais ameenda mbali zaidi katika kuhakikisha kwamba tunakwenda ku-protect viwanda vyetu vya ndani, amefanya jambo kubwa sana, kuna baadhi ya bidhaa ambazo zimekwenda kuongezewa tozo. Kwa kufanya hivyo nini tafsiri yake? Tafsiri yake ni kwamba, tunakwenda ku-discourage importation na kwa maana hiyo tunakwenda ku-stimulate uchumi ndani ili wazalishaji wetu waweze kuendelea. Kwa tafsiri pana ya kiuchumi maana yake ni nini, wale waliosoma commerce wanajua, hapa kinachokwenda kufanyika tunakwenda kufanya mitigation kwenye balance of trade ili twende kwenye balance of payment. Nimwambie tu Mheshimiwa Mwigulu, bajeti hii ni bajeti ya kisayansi zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba niendelee mbele. Pamoja na yote haya naomba niweke nukta zifuatazo vizuri zaidi. Mheshimiwa Waziri wakati ana-present bajeti hapa alizungumza suala la vijana wenye miaka 18 waanze kulipa kodi. Niki-quote hapa kwa ruhusa yako, kwenye chombo kimoja cha habari cha Global Publish kinasema, samahani na-quote:

“Waziri Mwigulu - kila Mtanzania mwenye umri kuanzia miaka 18 kuanza kulipa kodi”.

Mheshimiwa Spika, hii imeweza kuleta tafaruku kubwa katika mitandao, lakini Serikali na Mheshimiwa Waziri kwa nini namwambia bajeti hii imemfanya awe very popular Finance Minister, hapa kinachoenda kufanyika siyo kwamba mwanafunzi akifika umri wa miaka 18 alipe kodi. Determine factor hapa tunayoizungumza ni suala zima la kipato. Kwa hiyo kwa tafsiri hiyo, nilipa bahati ya kuishi kwa Wamakonde pale Uingereza, wao wanachokifanya, unapofika umri wa miaka 18 unapewa kitu kinachoitwa National Insurance Number Card, nini tafsiri yake? Tafsiri yake ni kwamba unapokuwa tayari ume-graduate umemaliza masomo, unapokwenda kufanya kazi tayari mfumo unakufahamu na hiki ndicho kilichoweza kufanyika katika bajeti hii. Kwa hiyo naomba niliweke hili liwe wazi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na haya yote, naomba vilevile niweze kuweka nukta nyingine sawa na nukta hii ninayoiweka sawa ni nukta inayohusiana na suala zima la Royal Tour. Mheshimiwa Rais amefanya kitu kikubwa sana katika kuifungua Tanzania, kwenye Royal Tour tunajua kwamba tunakwenda kupata mapato makubwa sana kule katika suala zima la utalii. Naiomba tu Serikali, Wizara husika zote lazima ziweze kuchukua nafasi yake, royal tour kama royal tour siyo kazi peke yake ya Wizara ya Utalii; Wizara ya Ardhi lazima sasa muweze kuhakikisha mnakwenda kupima ardhi katika maeneo husika ili wawekezaji wanapokuja siyo wanakwenda kwa Mwenyekiti wa Kijiji kwenda kuomba ardhi kwa ajili ya kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, kama hivyo haitoshi, Wizara vilevile inayohusiana na mambo ya Miundombinu lazima wahakikishe kwamba wanakwenda kufungua miundombinu katika sehemu tofauti, siyo mwekezaji anataka kwenda kuwekeza katika maeneo kama Kibiti maana yake Mukuranga sasa hizi kumeshajaa viwanda, watu wanaanza kuhangaika na mambo ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, si hayo tu katika Sekta nzima ya mambo ya Mawasiliano, pale ni lazima tuhakikishe tunakwenda kuweka mikonga ambayo itatusaidia. Wawekezaji watakapokuja siyo waanze kusumbuka, mtu kwenda kupiga simu anaenda kupanda katika mti halafu anaanza kupiga simu. Kwa kusema hivi niseme tu, Wizara husika lazima wayaangalie haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, vilevile Wizara ya Nishati lazima wawe makini kuhusu kupeleka umeme kwenye sehemu husika. Wawekezaji wanapokuja siyo tena tuanze kuhangaika kuchukua majenereta na kuanza kuwasha umeme.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya, naomba niweke jambo vizuri sana na hili ndiyo la msingi kwelikweli. Pamekuwa na chokochoko kidogo zinaendelea katika mitandao ya kijamii na suala hili linahusiana na suala zima la mambo ya Ngorongoro. Kwanza naomba niipongeze sana Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuweza kutenga eneo kwa wenzetu ambao wameamua kuhama kwa hiari kwenda kuishi katika maeneo ya Handeni.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, naomba niongee kwa dhati kabisa, sisi Watanzania wote kwa ujumla wake tunajua wafugaji waliopo katika eneo la Ngorongoro ni Watanzania wenzetu na hatukubali waweze kupata shida, lakini pia tunajua Serikali kama Serikali ina nia nzuri kabisa ya kulitatua tatizo hili amicably. Kwa hiyo naomba nisisitize, wale wenzetu majirani katika kipindi cha mwaka 1974 mpaka 1978, wakati huo akili yangu ilikuwa inafanya kazi, zilianza chokochoko kama mzaha hivihivi, kuna watu fulani fulani walikuwa wanataka kuchukua mipaka yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima kwa Kanuni zetu sitoweza kutaja jina la nchi yoyote ile, lakini niseme tu wale majirani zetu ambao wanajaribu kutuingilia katika mambo yetu ya ndani, wakome mara moja, hii hakubaliki. Hii ni Tanzania, sisi tuna uwezo wa kuamua mambo yetu ya ndani, hatuhitaji msaada wa kutoka sehemu nyingine yoyote ile. Inashangaza sana leo hii ukiangalia kwenye mitandao huko utakuta kabisa kwamba kuna maandamano yameandaliwa katika maeneo fulani ya majirani zetu. Sitaki kutaja jina, lakini niseme tu vita hii ni vita ya kiuchumi, Watanzania tuamke, Watanzania lazima walielewe hili, tuweze kushikamana na wenzetu waliopo Ngorongoro, tuweze kuisaidia Serikali ili tuweze kutatua matatizo yaliyopo mbele yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia katika Wizara hii ambayo ni muhimu sana. Awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yake kwa wasilisho zuri la bajeti ambayo walikuwa wamelileta mbele yetu ambalo linaweza kuleta matumaini kwa namna moja ama nyingine, ukizingatia kwamba kuna changamoto Wabunge wote tunafahamu katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja kwamba leo, nimeomba Mwongozo, imekuwa bahati kubwa sana kwasababu nimeweza kupata meseji kutoka kwa Meneja wangu wa TANROADS Mkoa akisema kwamba ndani ya wiki mbili zijazo ile Barabara ya Bungu – Nyamisati sasa inakwenda kutangazwa. Kwa tafsiri hiyo tunakwenda kumpata mtaalam kuanza hatua za awali za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri katika hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa tafsiri hiyo hiyo, japokuwa ulikuwa umetoa ushauri mzuri sana kwamba nibaki na mmoja, sasa kwa haya ambayo yameweza kufanyika naona wazi kabisa kwamba jambo lile la kupata mke wa pili linaanza kusogea karibu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishauri Serikali hasa katika miradi mikubwa mikubwa hii. Naomba niishauri Serikali kwa tafsiri kwamba miradi mikubwa mikubwa jana Mheshimiwa Reuben alikuwa amejaribu kuzungumza mambo ya finance model, ni jinsi gani tutakavyoweza kui-finance hii miradi mikubwa mikubwa. Ni ukweli uliokuwa wazi Watanzania tunahitaji maendeleo, ni ukweli uliokuwa wazi, Watanzania wana matumaini makubwa sana na Serikali ya Chama cha Mapinduzi, kwani mengi makubwa yameweza kufanyika katika awamu zote hasa katika Wizara hii. Makubwa sana yameweza kufanyika na sina shaka Awamu ya Sita vilevile inakwenda kuyafanya mambo makubwa na mazuri hasa katika Sekta nzima ya mambo ya Uchukuzi na Usafirishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri hasa katika Mradi wetu wa SGR. Katika mradi huu tuangalie financing model, kwa sababu mradi utakapokuwa umeweza kukamilika tafsiri yake pana ni kwamba tunakwenda kuhuisha matumaini upya ya Watanzania, sio tu katika maeneo ambayo yanapitiwa na mradi huo, lakini kwa Watanzania wote kwa ujumla wake. Kwa sasa tuweze kujaribu kuangalia, ndio maana naanza kurudia tena neno langu hili, lile suala la PPP lina shida gani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lilizungumzwa hapa Bungeni mwaka 2018 wakati sisi wengine tulikuwa hatua hata ndoto za kuja hapa Bungeni. Sasa shida iko wapi? Tujaribu kuangalia masuala haya kwa sababu tunapokwenda kukopa masharti yanakuwa mengi na Mheshimiwa Reuben amezungumza kwa kirefu sana na sidhani kama atakuwa ameeleweka vizuri. Alizungumza kwamba tunapokwenda kukopa tunapewa na masharti, wanatupa fedha na wakandarasi wanakuwa hao hao. Sasa sisi kama Serikali tujaribu kuweza kuangalia ni jinsi gani tunakwenda kuangalia suala zima la PPP na kuweza kukamilisha hii miradi mikubwa mikubwa. Huo ni ushauri wangu wa kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu wa pili kwa Serikali, naiomba sana Serikali, bahati mbaya sana ama bahati nzuri Wabunge sisi tunasoma hizi bajeti. Sio tu kwamba tukija hapa tunapiga makofi tunaondoka, hapana. Bajeti iliyokuwa imesomwa mwaka juzi, kuamkia mwaka jana, mwaka jana kuja mwaka huu kuna mambo yanakuwa yanaainishwa mle ndani. Wanavyosema kwenye bajeti hii kwamba upembuzi yakinifu umekamilika tunasubiri ujenzi, inasikitisha sana ukija tena katika mwaka huu tunaanza kumtafuta mtalaam wa kuweza kufanya upembuzi yakinifu. Tukifanya hivi tuna-send wrong signal kwa wananchi ambao wana matumaini makubwa sana na Serikali hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba sana kwa wale wataalam wetu ambao wanaandaa bajeti hizi, naomba twende tukatoe tahadhari kule kwamba Bunge hili la Kumi na Mbili, hawa watu wanasoma. Tunasoma hizi bajeti zinavyokuwa, tunapitia nyaraka moja hadi nyingine. Kwa hiyo, tukija hapa na majibu tunayoyategemea sio majibu ya kisiasa siasa. Tunategemea tupate majibu ambayo yanakwenda kwenye uhalisia ili sasa wananchi wale waliokuwa wametupigia kura kwa kishindo na Chama Cha Mapinduzi kikawa kimeingia madarakani waendelee kuwa na matumaini na nchi yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho naomba nizungumze, pamoja na uhalisia kwamba tayari nanyemelea kupata mke wa pili kwa sababu ya ile barabara ya Bungu – Nyamisati, pale kwetu vile vile kuna barabara ya kutoka Kibiti – Demani kwenda kule Mloka. Hii ni barabara muhimu sana kwa sababu kule ndiko mradi ule wa Mwalimu Nyerere unafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali, najua pamoja na mambo makubwa na mazuri ambayo tayari tumeshayafanya kama Serikali katika Sekta nzima ya Mambo ya Ujenzi na Uchukuzi lakini vile vile tuangalie. Nimewasifia hapa kwamba imefanya vizuri, sina maana kwamba eti kwa sababu Kibiti haikuwekewa bajeti ile nisiseme kwamba mmefanya vizuri, hapana! Mmefanya vizuri sana lakini tuweze kuangalia vile vile uwezekano wa kuweza kupatikana fedha za dharura ili pale watu wa Kibiti na Demani kule ambako wananchi wangu wanakohoa sana kwa vumbi na malori yanayopita pale kwa kupitia mizigo ile inayokwenda kule kutengeneza mradi ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ikiwezekana Mheshimiwa Waziri ungekaa na wataalam wako kama kuna ka– emergency kule pembeni basi kaweze kutoka kale kafedha uweze kwenda kufanyika hatua za awali za upembuzi yakinifu ili sasa tuweze kuangalia jinsi gani tutakavyoweza kuokoa wananchi wale kuondokana na matatizo ya kifua wanayoyapata. Magari mengi sana yanapita pale, na haya mambo ukiona mtu mzima anapiga piga kelele, kuna jambo, Mheshimiwa Aweso huwa anasema hivyo. Ukiona mtu mzima anapigapiga kelele, kuna jambo, Mheshimiwa waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, amezungumza hapa jana, alisimama kwa mara ya kwanza sikutegemea. Alisema kutoka pale Mbeya kwenda Tunduma kapata kilometa tano ndani ya miaka 6. Haya mambo ya kuona sana, sasa mtu mzima akiwa amesimama hivi, kuna jambo. Ninavyozungumza kwamba jamani nawataka wale wake wanne, liko jambo! Wazee wameniahidi wale kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri sitaki wewe mchawi wangu. Najua utalifanya hilo na nina imani sana na Serikali hii ya Chama Cha Mapinduzi hasa Serikali ya Awamu ya Sita kwa mambo makubwa na mazuri ambayo yanakwenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia katika Wizara hii ambayo ni muhimu sana. Kwanza kabisa nichukue nafasi hii kuipongeza Wizara ya Kilimo kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya kwa muda mrefu tangu nchi hii ipate uhuru.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika maeneo makubwa mawili. Eneo la kwanza litakuwa ni eneo A, hili litakuwa linahusu Mkoa wa Pwani na eneo la pili tutakuwa tunazungumzia suala zima la Kitaifa na imani yangu ni kwamba dakika tano zitatosha sana.

Mheshimiwa Spika, nina masikitiko makubwa sana katika bajeti ambayo imetoka kuzungumzwa katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri kwamba bajeti hii haikuugusa Mkoa wa Pwani kama vile ipasavyo. Ni masikitiko yangu makubwa sana kuona kwamba pale Pwani katika Wilaya ya Rufiji watu wa Kibiti sisi ni wahusika, watu wa Mkuranga ni wahusika. Kuna mradi mzuri sana pale katika Bwawa la Mwalimu Nyerere lakini bajeti/hotuba hii haikuzungumza chochote kuhusiana na suala zima la kilimo cha umwagiliaji sijui, sisi watu wa Kibiti, Pwani, Rufiji tumekosa nini kwa Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kama hivyo haitoshi masikitiko yangu mengine makubwa ni kwamba watu wa Pwani hasa watu wa Kibiti, Rufiji, Mkuranga, Kisarawe, Bagamoyo, Mafia sisi ndiyo wakulima kule wa zao la korosho wakizingatia kwamba pale Kibiti ndiyo barabara yao. Tunazalisha korosho kwa wingi sana. Tuna shida sana sisi pale Pwani kuhusiana na ubora wa korosho zetu na suala hili tumekuwa tukilijadili mara kwa mara. Waheshimiwa Wabunge tukiwa tunakutana na Mheshimiwa Ulega, Mheshimiwa Mchengerwa pamoja na Mheshimiwa Jaffo tulikuwa tunakaa tunajadili suala hili, jinsi gani tutakavyoweza kusaidia sasa Serikali ili iweze kutusaidia. Zao hili la korosho liwe na ubora wa kutosha kwa sababu kila mwaka zao hili pale Pwani bei yake iko chini zaidi.

Mheshimiwa Spika, grade A, inayokuwa inauzwa kule kwa watoto wetu Kusini, pale Pwani inauzwa mpaka shilingi 400, hiki kitu hakieleweki. Nasikitika sana Profesa katika hotuba yako hujaeleza mkakati gani mlionao ili kuweza kutusaidia sisi watu wa Pwani, ili ubora wa korosho zetu uwe mzuri na vilevile tuweze kupata bei ile ambayo inastahiki kama vile watoto wetu wa Kusini na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nataka nichangie ni la kitaifa zaidi. Hotuba hii haijajibu maswali ya msingi ya mkulima; leo mkulima anahitaji soko na sustainability ya price. Mheshimiwa Waziri amekuja hapa hakutuambia mikakati gani Wizara au Serikali inayo katika kuhakikisha kwamba wakulima wa korosho, ufuta, pamba na wakulima wa mazao mengine na kwa ndugu zangu hapa Wagogo, wana mkakati gani kuhakikisha tunapata soko. Tulikuwa tunategemea Serikali mnavyokuja hapa na hii bajeti, mnakuja kusema mipango kwamba tuna mpango moja, mbili, tatu wa kuweza kupata masoko. Mkulima huyu anakwenda kulima soko hamna mnategemea kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la pili la kusikitisha ambalo hili ni majonzi makubwa vilevile, Serikali haijaja na mpango wa kuweza kutuambia ni jinsi gani sasa wanaanza kufikiria jinsi ya ku-control price ya mazao haya. Wakulima wanapata shida kubwa sana, wanalima na kuuza katika mazingira magumu sana na wanavyouza vilevile price inayopatikana siyo ya kufurahisha, lakini malipo yenyewe vilevile hayapatikani kwa wakati. Tulikuwa tunategemea Serikijali ikija hapa mnakuja na mpango wa kutuambia kwamba katika bajeti hii mmejipanga kuweza kuona price inakwenda juu na vilevile wakulima wanakwenda kulipwa kwa wakati, lakini hilo halikuweza kuzungumzwa katika hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine cha kusikitisha zaidi hotuba hii haijagusa hata kidogo suala zima la matatizo ya ushirika. Sisi tulikuwa tunategemea kwamba Waziri akiwa anakuja hapa anakuja kutueleza kwamba jamani ushirika kule tunajua kuna matatizo kwa hiyo sisi kama Serikali tumejipanga sasa kwenda kufanya 1, 2, 3 ili kumkomboa mkulima huyu.

Mheshimiwa Spika, nataka nikwambie sisi katika Mkoa wa Pwani tuna kitu kinaitwa CORECU, ni shida. Tulikuwa tumekaa Wabunge sisi tukajadili, Mheshimiwa Ulega akiwepo, Mheshimiwa Mchengerwa na Wabunge wengine ambao tuko katika Mkoa wa Pwani, tumekwenda mpaka tukafikia hatua kwamba tumebadilisha uongozi katika CORECU ili kuweza kuona jinsi gani tunakwenda kumsaidia mkulima. Cha kusikitisha zaidi Serikali hamjaja na mpango halisia wa kutuambia ni jinsi gani mnakwenda kutatua kero ya mkulima wa pamba, kahawa, korosho, ufuta, katika suala zima la ushirika. Wabunge wengi wamesimama wamezungumza suala hili.

Mheshimiwa Spika, lakini lingine kubwa zaidi la kusikitisha, Serikali hamjaweza kutuambia mnafanyaje kuhusiana na ile interference katika suala zima la agriculture. Interference ina shida, mturuhusu sisi tulime.

Mheshimiwa Spika, without prejudice na kwa heshima na taadhima ya hali ya juu, sisi wakulima hatutegemei leo eti uende ukampe kishkwambi hicho Afisa Ugani aende kule chini Mchukwi, Ruaruke, Kipugila, Mkuranga kumsimamia mkulima, hiki kitu kinatoka wapi? Tuna data base ambayo tumeshaiandaa sisi kama Serikali, hakuna. Leo Mheshimiwa Waziri nikikuuliza kwamba tuna wakulima wangapi Tanzania you haven’t got a clue.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Ally Mpembenwe dakika zako zimekwisha, lakini kwa dakika moja tu kabla hujakaa chini ulianza kwa kuwalaumu kidogo kwamba hawakuwa na mpango wowote kuhusu umwagiliaji kuhusiana na Bwawa la Mwalimu Nyerere, sikukuelewa hapo unataka kusema nini?

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mradi ule wa Bwawa la Mwalimu Nyerere unakwenda sambamba na mradi mzima wa umwagiliaji. Sisi watu wa Kibiti, Rufiji, Mkuranga, kuna ardhi nzuri kule tunategemea masuala ya hot culture yaweze ku-take place. Serikali hawajaja na mpango wa kueleza kwamba Bwawa hili la Mwalimu Nyerere mbali ya kwamba linakwenda kutoa umeme lakini vilevile linakwenda kuwasaidia wananchi kule katika zile ekari 150,000 kuweza kuwa na kilimo cha umwagiliaji. Hii ilikuwa ni concern yangu kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia katika Wizara hii ambayo ni muhimu sana katika mustakabali mzima wa uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia, nilikuwa naomba nichukue fursa hii kwanza kabisa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri wake kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameendelea kuifanya kwa muda mrefu sana katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nichukue fursa hii kukupongeza wewe mwenyewe binafsi, hicho kimekupendeza kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu umegawanyika katika sehemu kubwa mbili; nitachangia Kitaifa halafu nitarudi pale Jimboni kwangu Kibiti ambapo tuna matatizo makubwa sana ya msingi katika sekta hii au katika Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuwa nimepitia vizuri zaidi hotuba ya Mheshimiwa Waziri, haikuweza kutueleza kwa kina zaidi katika baadhi ya maeneo fulani fulani, lakini naomba niguse maeneo mawili tu. Eneo la kwanza nitagusa katika suala zima la utalii wa ndani, halafu eneo la pili, nitagusa katika suala zima la country tourism.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala zima la utalii wa ndani, Mheshimiwa Waziri katika hotuba yake hakutuambia hasa mikakati ya Serikali au mikakati ya Wizara; nini tunachokwenda kukifanya ili kuweza kuhakikisha utalii wa ndani vile vile nao unakwenda kuchangia katika pato la Taifa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona kuna mambo mengi sana yamefanyika, mengi yameelezwa, mojawapo ikiwa ni suala la Simba kuweza kuitangaza Tanzania, “Visit Tanzania.” Swali ambalo tunapaswa tujiulize, tufanye evalution kwamba Visit Tanzania imetusaidia nini katika suala zima la utalii? Kwa sababu tunaweza tukafanya advertisement nyingi sana, lakini at the end of the day, lazima tujue hizi advertisement ambazo tunazifanya tunazi-evaluate vipi? Tunazi-quantify vipi in terms of hawa watalii na fedha ambazo zinakuja kutumiwa na watalii? Hili ni suala la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nitegemee tu kwamba wewe pamoja na wataalam wako mkiwa mnakaa katika mikakati ambayo inakuwa inaendelea katika kuweza kuboresha masuala mazima ya internal tourism, hizi activities tunazozifanya lazima tufanya self-evaluation, zimesaidia vipi? Hili ni suala la msingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala zima la hunting tourism. Naomba niguse pale ambapo Mheshimiwa Nape alipokuwa amegusa asubuhi kwamba kuanzia mwaka 2013 na kuendelea mapato yale yaliyokuwa yanapatikana katika suala zima la hunting tourism yamekuwa yakipungua kidogo kidogo. Tumeambiwa mwaka 2013 tulikuwa tunapata mpaka dola milioni 27, lakini todate tunazungumzia kwenye Dola milioni nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu, mfumo wa kugawa vitalu hauna shida, uko vizuri kwangu mimi, kwa sababu Serikali walikuwa wamechukua maamuzi hayo kwa kwa kuzingatia kwamba tunakwenda kutokomeza mambo yale ya ubadhilifu yaliyokuwa yanafanyika kwenye vitalu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha msingi zaidi cha kufanya nafikiri kuna kitu kimoja hapa lazima tukiangalie. Kwenye economics kuna kitu kinaitwa law of demand na law of supply. Kwenye law of demand tunaamini kwamba the higher the demand, the higher the price; na kwenye suala zima la law of supply tunaamini kwamba the highest supply, basi the low the price if other factors zinakuwa zina-remain constant. Tuelewe tu, hapo hapo kwenye economics, kuna kitu kinaitwa product substitutes, yaani kama kuna product fulani ambayo inaendana na product nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wataalam wetu kitu ambacho wamejisahau, tulitoka kwenye Dola 7,000 katika kuuza vitalu hivi, tukaenda kwenye Dola 30,000, sasa hivi tuko kwenye Dola 80,000. Tumeambiwa kwamba tuna vitalu karibia 40 vyote hivyo viko katika mazingira kwamba havina watu na vingine 14 viko katika hali mbaya sana. Tafsiri yake ni kwamba, twende kwenye basics za economics kwamba pale ambapo pana demand ya hali ya juu sana. Ni mategemeo yetu kwamba sisi tunaweza kukaviuza vitalu hivi kwa bei ya juu, hakuna shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke tu kwamba, sisi tuna competitors wetu vile vile. Ni vyema zaidi katika sekta hii ya hunting tourism lazima tuweze kufanya kazi ya ziada ili sasa kuweza kufahamu competitors wetu wana-add value vitu gani vinavyoweza kuwavutia wale watu wanaokwenda kuwinda kule? Maana yake ni nini? Ni kwamba vitalu tunavyo, nasi Tanzania we are biological reach, lakini very unfortunately tunashindwa kuutumia huu utajiri tuliokuwanao vile ipasavyo. Namwomba tu Mheshimiwa Waziri akae na wataalam wetu, ili sasa tuweze kujua ni kitu gani ambacho wenzetu wanakifanya ili nasi vile vile tuweze kufanya tuweze kuwavutia watu waje kuwekeza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hilo, nilikuwa naomba vilevile niguse katika sehemu nzima ya mambo ya mapato. Mheshimiwa Waziri ametuambia kwamba kuna fedha tunakusudia kuzikusanya katika mwaka wa fedha huu karibia shilingi bilioni 478.01 katika sekta yetu kule TAWA, Ngorongoro, hizi fedha zote zinakwenda moja kwa moja kule TRA. Ni vyema sasa wangeweza kutuambia mikakati gani ambayo tunakwenda kuifanya ili kuweza kufikia lengo hili? Vinginevyo tunaweza tukawa tunazizungumza hizi namba lakini tafsiri pana ni kwamba, tunaweza tukawa tunashindwa kufikia malengo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nilikuwa naomba sasa niende jimboni kwangu. Mheshimiwa Waziri naomba tusikilizane vizuri sana hapa. Wewe ni rafiki yangu, mtani wangu, maana unatokea kule kusini kusini; na mkae mkijua kwamba sisi ndio tuna barabara pale. Mkiwa mnaleta taabu Mheshimiwa Waziri unaweza ukashindwa kuja Dodoma huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo moja la msingi sana kule. Serikali mwaka 2017/2018 ilifanya zuio kwa makusudi mazima, tena mazuri zaidi ya kuweza kulinda mazingira jinsi ya uvunaji wa mikoko. Mwaka 2019 Serikali ilituma wataalam ili sasa kwenda kufanya tathmini, mikoko ile itaenda kuvunwa vipi na kuweza kulinda mazingira? Mwaka 2020 wataalam wale walikuja katika maeneo husika, maeneo mengi sana ambayo yanazungukwa na maziwa pamoja na mito ili kuja kuwaeleza kwamba tathmini imeshakamilika na kwa namna moja ama nyingine Serikali itatoa tamko ni jinsi gani sasa mikoko ile itawezwa kuvunwa ili tusiweze kuharibu mazingira?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Waziri, kule kwangu mimi kuna maeneo ya delta, nina kata kama tano; kuna Kata ya Kiongoroni, Kata ya Maparoni, Kata ya Mbochi, Nsala, Salale; vile ni visiwa. Hii mikoko ni mali tuliyopewa na Mungu, tunajua lazima tulinde mazingira. Sasa ni jambo la msingi tuweze kujua ni jinsi gani wananchi wale wanakwenda kuokoka katika kuivuna mikoko hii. Kwa hiyo, ni mategemeo yangu Mheshimiwa Waziri, utakapokuja kufanya wind-up hapa, uje kutupa tamko la Serikali, nini tunachoenda kukufanya ili wananchi wale waruhusiwe kuivua mikoko ile? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili na la msingi ni suala zima la wajasiriamali wangu pale Kibiti. Kuna wajasiriamali hawa ambao wanafanya shughuli za randa hizi. Inasikitisha sana, wananchi wale tunawaita wajasiriamali, wanatengeneza vitanda na vitu vingine, lakini cha kusikitisha tu ni kwamba tozo ambazo wanatozwa ni nyingi sana. Kuna urasimu wa hali ya juu kiasi kwamba watu hawa wanashindwa hata kuweza kufanya shughuli hizo.

Kwa hiyo, naomba wa Kihesa wanaenda kulipa TFS, ambayo inawachaji shilingi 55,000/=. Kuna tozo wanaenda kulipa TRA, kuna tozo wanaenda kulipa Halmashauri, kuna tozo wanakwenda kulipa katika vijiji husika. Sasa hawa wajasiriamali tunawasaidia vipi? (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Haya, ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuchangia taarifa ambayo imewasilishwa mbele yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia taarifa hii kwanza nilikuwa naomba nichukue nafasi hii kukupongeza kwa kuchaguliwa kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Lakini sambamba na hilo nimpongeze Mheshimiwa Rais mama yetu Samia Suluhu Hassan jinsi anavyoweza kuendelea kufanya kazi kupeleka fedha katika halmashauri zetu zote nchini na kuweza kuona maendeleo yanakwenda kufanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kipekee nishukuru fursa hii kuwapongeza Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwa kazi kubwa na nzuri ambazo wanazifanya ili kuweza kusimamia fedha hizo. Sambamba na hilo shukrani za dhati kabisa ziende kwa Mkuu wangu wa Mkoa wa Pwani, Alhaji Abubakar Kunenge kwa kusimamizi wake mzuri kabisa wa fedha katika Mkoa wa Pwani na Wilaya zote kwa ujumla wake. Lakini bila kumsahau Mkuu wangu wa Wilaya Kanali Ahmed Abbas kwa kazi kubwa na nzuri wambayo anaifanya ndani ya Jimbo la Kibiti katika kuweza kusimamia halmashauri, miradi ya maendeleo na fedha vilevile ndani ya halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni mjumbe wa Kamati la LAC, kwa hiyo, nimesimama hapa kuchangia taarifa iliyokuwa imewasilishwa na Mwenyekiti wangu mama Grace Tendega ambayo imewasilisha taarifa hiyo in very majestic way. Ahsante sana Mheshimiwa Mwenyekiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie nukta mbili tu, lakini katika nukta hiyo nitaigusa sana katika sehemu nzima masuala ya upotevu wa mapato ndani ya halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, tumeona ndai ya taarifa yetu lakini tumeona vilevile wakati tulipokuwa tunafanya suala zima la ukaguzi na kuwahoji wale maafisa masuhuli. Kuna upotevu mkubwa sana wa mapato ya ndani ukizingatia kwamba mfumo unaotumika wa POS unautata mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inatokea halmashauri moja au nyingine siku karibia 254 mashine ya POS inakuwa iko off, halafu hakuna taarifa zozote za kifedha ambazo zinaweza zikasoma katika halmashauri husika au kule TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbali ya hiyo kuna tatizo lingine la msingi ambalo linapatikana katika upotevu wa fedha, tatizo hilo ni kwamba kuna kitu kinaitwa adjustment. Watu wa halmashauri wanachokifanya ni sawasawa kwamba mtu amekwenda kukatiwa risiti ya shilingi milioni moja, halafu baadae anakuja kufanya adjustment kwamba amekata risiti ya shilingi laki moja. Katika taarifa ambayo ilikuwa imesomwa na Mwenyekiti wangu hapa fedha takriban shilingi bilioni 4.5 zimeweza kuonekana zimefanyiwa adjustment katika kipindi cha mwaka 2019/2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini ushauri wangu, ushauri wangu kwa Serikali kuna shida pale katika kitengo cha TEHAMA – TAMISEMI, lazima suala hili liweze kushughulikia kwa sababu haiyumkiniki halmashauri 35 adjustment zilizokuwa zimeweza kufanyika bilioni 4.5 kama zingekuwa halmashauri zote 86 zingeweza kufanyika adjustment za kiasi gani. Kwa hiyo, pale TAMISEMI katika Kitengo cha TEHAMA kuna tatizo la msingi zaidi. Kwa hiyo, ni vema Serikali muweze kuangalia nini mnachoweza kukifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini katika eneo lingine ambalo nilikuwa naomba nitoe ushauri. Kuna shida kubwa kidogo kwa wataalam wetu katika suala zima la kuweza kuwasilisha mahesabu au kuandaa mahesebu. Wataalam hawa tunajua wana professional zao, lakini nilikuwa naomba kuishauri Serikali waendelee kuwafanyia training kwa sababu wanachokuwa wanakifanya zile financial statement ambazo zinakuja zinakuwa na mapungufu mengi sana; na kwa tafsiri hiyo hiyo maana yake ni nini? Inakwenda kusababisha madhara kwa watumizi wengine wa financia statement. Kwa hiyo, nilikuwa naishauri Serikali waweze kuangalia uwezekano ni jinsi gani watakavyoweza kufanya training kwa wataalam wetu ambao wanafanya shughuli hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo lingine la msingi zaidi ambalo nilikuwa naomba nilichangie, halmashauri zetu nyingi sana zina madeni. Na madeni haya yanasababishwa na suala zima la uandaaji wa financial statement. Kwenye accounts kuna kitu kimoja kinaitwa massaging the figure au window dressing, wanachokuwa wanakifanya ni kwamba financial statement inaandaliwa inakwenda kuwa-impress other users ambao wanakuwa kama vile financial institution. Halmashauri inatoka inakwenda kuomba mkopo, lakini kutokana na kwamba ile financial statement imechezewa, kinachofanyika pale ni kwamba wanakwenda kupata mkopo, ambapo mkopo huo hawawezi kuumudu. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo maana yake ni nini? Tunaziweka halmashauri katika matatizo mengi sana ya msingi. Halmashauri nyingi sana zinakuwa zinakesi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa heshima na taadhima na unyenyekevu wa hali ya juu kabisa naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuichangia hotuba hii ya Waziri wetu wa TAMISEMI. Kabla sijaanza kuchangia hotuba hii naomba kwanza nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya ndani ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile nichukue fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Manaibu Waziri wanafanya kazi nzuri kwelikweli. Waziri huyu siku zote mabega yako chini na mimi niseme tu Mawaziri wengine mchukue mfano huu. Kijana huyu unampigia simu anapokea, kama akiwa kwenye kikao nipo kwenye kikao halafu anakupigia, lakini sijawahi kumuona hata siku moja akikasirika, yeye anakasirika akiwa field kule akiwa anazungumza na Wakurugenzi pamoja na Watendaji wa Halmashauri. Mheshimiwa Waziri piga kazi na Naibu Mawaziri safi sana hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa mambo makubwa na mazuri ambayo ametufanyia sisi watu wa Jimbo la Kibiti. Mheshimiwa Rais alitafuta fedha takriban shilingi trilioni1.3, katika fedha hizo najua ziligawiwa Tanzania nzima katika sekta nzima ya elimu shilingi bilioni 662.32.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kibiti vilevile humo tumo, tumepewa fedha Shilingi Milioni 470 tunajenga shule ya Sekondari pale. Kama hivyo haitoshi tumepewa fedha shilingi 1,480,000,000 tumejenga madarasa takriban 74, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais katika eneo hilo. lakini kama hivyo haitoshi Mheshimiwa Rais vilevile ametupa fedha shilingi milioni 100, tumejenga bweni kwa vijana ambao wana mahitaji maalum. Safi sana Mheshimiwa Rais nami sina budi kusema nani kama Mama Samia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, katika sekta nzima ya afya mimi najua kuna fedha zilizokuwa zimeanza kutolewa takribani shilingi bilioni 241.41 katika fedha hizo nasi Kibiti vilevile tumo. Tumepewa fedha takribani shilingi milioni 500, tumejenga pale kituo cha afya kizuri katika Kata ya Mjawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hivyo haitoshi tumekwenda vilevile kujenga nyumba za Watumishi kule katika Kata ya Ngw’aluke pale Nyamatanga, kwa Diwani Bingwa kabisa Ndugu yangu Mkenya kazi nzuri sana inakwenda kufanyika na Mheshimiwa Rais. Nani kama Mama Samia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee, tunafahamu vilevile katika fedha hizo kuna fedha ambazo Mheshimiwa Rais ameweza kututafutia sisi watu wa Jimbo la Kibiti. Tumepewa fedha katika kujenga zahanati, tumejenga zahanati kule kwetu Mbuchi, Mtawanya, tumekwenda kujenga zahanati katika Kata vilevile ya Mjao. Tumepewa vilevile fedha Shilingi Milioni 50, tumejenga zahanati katika Kata ya Kibiti, nani kama Mama Samia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee mbele. Katika fedha hizi vilevile kuna fedha za TARURAambazo zimetolewa Bilioni 597, katika fedha hizo nasi Kibiti vilevile tumo. Tumepewa fedha takribani Shilingi Bilioni 200 lakini kubwa kuliko yote Mheshimiwa Rais ameweza kutupa fedha takribani shilingi bilioni 6.2. tumejenga daraja pale Mbuchi, daraja zuri kabisa leo hii wananchi wa Mbwera wanaweza wakaja Kibiti na kuja Dar es Salaam na wakalala Mbwera bila shida yoyote. Nani kama Mama Samia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi, nilikuwa naomba nitoe changamoto zilizopo ndani ya Jimbo langu. Nikianza katika sekta ya afya. Katika Jimbo langu nina shida pale kidogo kuna Kituo cha Afya kilichopo katika Kata ya Mwambao, kuna Kituo cha Afya kilichokuwa katika Katika ya pale Mbuchi. Vituo vya Afya hivi vimeshakamilika; lakini mpaka hivi leo ninavyozungumza hatuna vifaa tiba, tuna uhaba wa watumishi vilevile, kama hivyo haitoshi tuna zahanati kule Kiongoloni, Mbwera mpaka Maparoni hatuna Watumishi. Mheshimiwa Waziri hili naomba uliangalie kwa karibu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jambo lingine ambalo vilevile naomba nilichangie. Sasa naomba nitoe ushauri pale TAMISEMI. TAMISEMI pale kuna shinda, shida iliyopo kubwa zaidi ipo kwenye suala zima la ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri. Tuna mfumo unaoitwa mfumo wa POS; mimi nipo katika Kamati ya LAAC, katika taarifa ya CAG ya mwaka jana fedha ambazo zilikuwa zimefanyiwa adjustment ni takribani Bilioni 4.5, fedha hizi zimefanyiwa adjustment na huu ni wizi wa hali ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu anayekusanya mapato kule chini, amekusanya labda Shilingi Milioni Moja, halafu anakuja kufanya adjustment inaandika Shilingi 10,000 huu ni wizi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba liangalie hili kwa karibu sana kwa sababu tusipofanya hivyo tunakwenda kupoteza fedha nyingi sana kule katika eneo zima la ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo lingine ambalo naomba nitoe ushauri wa hali ya juu TAMISEMI ni kuweza kuangalia ni jinsi gani ya kuweza kudhibiti mapato ndani ya Halmashauri zetu. Kuna shida kubwa tena kuna shida kubwa ya msingi kwa sababu kinachokuwa kinafanyika mapato yanapigwa, kuna Watendaji ambao siyo waadilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba mtengeneze mfumo ulio halisia ili sasa kuweza kuhakikisha mnakwenda kudhibiti mapato ndani ya Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba kulizungumza hapa kidogo nitakwenda tofauti na Waheshimiwa Wabunge wenzangu. Kuna baadhi ya Wabunge wenzangu wameweza kuchangia kwa heshima kubwa kwamba posho za Halmashauri ziende equal kwa kila Majimbo. Hapa kuna shida!

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwangu nina Kata zipo kule Visiwani kabisa, kuna Kata ya Kiongoloni, Maparoni, Msala na Salale, ili Diwani kutoka kule kuja katika Makao Makuu ya Halmashauri kuja kufanya shughuli za Halmashauri maana yake ni kwamba lazima atumie siku mbili.

Mheshimiwa Waziri kila mtu ale na umbali wa Kamba yake kwa tukifanya hivyo tutakuwa tunawatendea haki hao Madiwani. Tena mimi ikiwezekana katika Halmashauri yangu suggest tu Taifa zima, tuweze kuweka utaratibu Madiwani hawa wapatiwe mpaka vyombo vya usafiri wanafanya kazi kubwa kweli, tukifanya hivyo tunakwenda kutetea maslahi mapana ya Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hivyo haitoshi tunakwenda vilevile kutetea maslahi mapana ya kuweza kusuma maendeleo. Sisi Wabunge tupo huku, muda mwingi sana tunakuwa tupo katika Vikao vya Bunge, wao wapo kule ndiyo wanasimamia shughuli za kimaendeleo, kwa hiyo, tusipowawezesha hawa inakuwa shida tena ni shida ya msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili kuweza kuchangia hoja hii ya msingi zaidi iliyopo mbele yetu. Awali ya yote niseme naunga mkono hoja, lakini la pili nashukuru jitihada ambazo tayari zimeshachukuliwa na Serikali katika kuweza kuangalia jinsi ya kuweza kutatua tatizo hili.

Mheshimiwa Spika, kwenye uchumi kuna tools maalum ambazo huwa zinatumika kwenye kuweza ku-regulate uchumi wa nchi. Kuna kitu kinaitwa monetary policy na kuna kitu kinaitwa fiscal policy sasa kwa interest ya muda mimi nilikuwa naomba niizungumzie hii fiscal policy kwa kifupi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana Waziri Mheshimiwa January Makamba mdogo wangu big up na hii inanikumbusha sana kauli ya Mzee Kikwete anaposema kwamba big brain lazima tuweze kuzipa nafasi yake.

Mheshimiwa Spika, kulikuwa na wazo la tozo ile la kusema Sh.100 tunaipunguza ili kuweza kuangalia hali kidogo ya mafuta itakavyokuwa, lakini for some reasons the situation was very ballistic, kwa hiyo kukawa na interpretation tofauti. Sasa hapa kwenye fiscal policy ndio sehemu ambayo sasa Serikali inapaswa ipafanyie kazi ya msingi. Wabunge wenzangu wamezungumzia suala hapa la kwenda kukopa, lakini naomba nitoe ushauri kwa Serikali naishauri Serikali isiende kukopa kwa ajili ya kutatua tatizo hili, no. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachoomba kuwashauri Serikali ni kwamba, tozo zilizopo katika mafuta zipo takribani 23 tozo moja tu la Sh.100 ambayo ilikuwa imetolewa, najua kilikuwa kina athari na sisi bajeti yetu ni cash budget system kwamba tunakusanya halafu tunatumia na hizi tozo tayari tumeshaziweka katika mahesabu yetu kwamba tunakwenda kuzitumia. Sasa ushauri wangu kwa Serikali ni lazima tuangalie vyanzo vipya vya mapato. Nilitoa mfano hapa mwaka jana kwamba twendeni tukaangalie jinsi gani ya kuweza kuwa na kitu kinaitwa TVA License viewers wa TV wako wengi sana na ni chanzo cha mapato kinachojitegemea.

Mheshimiwa Spika, leo mama anakwenda kukopa fedha kwa ajili ya kuweza kuleta mambo ya maendeleo ndani ya nchi, tumeona mambo ya madarasa, tumeona vituo vya afya na hili vilevile tumwombe Mheshimiwa Rais kwenda kukopa? Nasema tu kwa Wabunge wenzangu, mawazo yangu ni kwamba tuangalie vyanzo vipya vya mapato. Hapa ndipo sasa Wizara ya Fedha inapaswa iangalie nini cha kuweza kufanya, ndio maana tuna kitu tunaita Wizara ya Fedha na Mipango. Hizi brain kubwa kubwa za late kina Profesa Ngowi ziko wapi. Huu ndio wakati muafaka sasa wa kuangalia kipi kinaweza kufanyika kwenye fiscal policy, pale ambapo kuna gap ya fedha tunazozitoa kwenye tozo… (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mpembenwe kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nataka nimpe taarifa tu mzungumzaji kwamba, hapa tunaongelea jambo la dharura kuweza ku-rescue hii situation ya mafuta, anapendekeza vyema anasema kwamba, tuangalie vyanzo vipya vya mapato ambavyo itategemea mpaka tunamaliza Bunge la Bajeti. Sasa hiyo inakuwa haina udharura wowote ule, ukipendekeza chanzo kipya cha mapato sasa hivi lazima kije hapa Bungeni tukiidhinishe na kitakuja kupitishwa kwenye Sheria ya Fedha ambayo tunaitengeneza mwaka huu. Kwa hiyo, ni jambo la dharura tunaomba ujielekeze vyema. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, uchumi ninaouzungumza hapa ni uchumi wa hali ya juu sana, too advanced to be understood by ordinary individual. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapozungumza kutoa tozo maana yake ni nini Serikali, Wizara ya Fedha na Mipango sasa ni wakati muafaka wa kuweza kuangalia kama tuliweza kusema kwamba tumetoa Sh.100 tukawa na deficit ya shilingi bilioni 30 tunajaribu kuangalia where are we going to get that money from? Tunapoweza kujua kwamba wapi tunakwenda kuipata hiyo fedha, ndio pale tunakuja na tafsiri sasa fiscal policy inakwenda kufanya kazi na kwa tafsiri hii hii maana yake ni nini, tusiwe tunakwenda kwenda tu katika kukopa kopa, tunakwenda kukopa ndio sawa, kuna mambo ya kwenda kufanyika kwa ajili ya kukopa, lakini kuna technics za kiuchumi ambazo inabidi sasa ziweze kufanyika na the brain inayoweza kutumika ni Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, nimezungumza hapa suala vile vile la mambo ya monetary policy, hili ni suala ambalo linajitegemea tofauti, lakini Waheshimiwa Wabunge wenzangu sidhani kama tumeweza kuligusa kwa undani zaidi... (Makofi)

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Mpembenwe kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Agnes Mathew Marwa.

T A A R I F A

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba ni kweli suala la kukopa kwa sasa hivi kwa suala hili la dharura kwanza kukopa ni process, lakini pia ni kuhamisha tatizo kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine ambao mzigo huo huo utarudi kwa wananchi. Ijapokuwa kukopa ni suala zuri, lakini sasa kwa sababu hili ni suala la dharura basi tuangalie jinsi tu ya kuondoa hizo tozo chefuchefu ambazo zitasaidia kwa sasa hivi kwa suala la dharura. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Agnes nadhani Mheshimiwa Mpembenwe alisema yeye haungi mkono hilo eneo la mkopo. Sasa ni kwamba unampa taarifa au unamuunga mkono kwenye hoja yake kwamba yeye hakubaliani na hoja ya kwamba nchi ikope?

MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, namuunga mkono.

SPIKA: Mheshimiwa Twaha Mpembenwe.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, ndio maana huyu ni kada mzuri wa Chama cha Mapinduzi, napokea taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninachotaka kusema tu ni kwamba Serikali sasa, Wizara ya Fedha na Mipango ni wakati muafaka sasa wakae kitako na kuweza kuangalia vyanzo vipi tunakwenda kuvitumia ili kuweza ku-rescue situation. Kwa tafsiri hiyo hiyo maana yake ni nini? Narudia kusema kwamba Mheshimiwa January wazo lake lilikuwa zuri sana, lakini hakuweza kueleweka, it was too advanced, probably the procedures hazikuwa za kufuatwa the way it should be lakini at the end of the day twendeni tukaondoe hizi tozo zilizopo. Tozo
23 katika suala zima la mafuta this is absolutely ridiculous. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naona kengele imegonga, naunga mkono hoja, lakini tusiende kukopa Wizara ya Fedha wakae kitako. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia. Kwa ufinyu wa muda nianze tu kwa kumshukuru kwanza Mheshimiwa Rais kama amiri jeshi mkuu kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya ndani ya nchi ili kuweza kuhakikisha kwamba vyombo vyetu vyote vya usalama vipo shwari na raia tupo salama vilevile. Pili nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaendelea kuifanya katika jeshi la polisi. Nitakuwa mchoyo wa fadhila; nimpongeze sana Afande IGP Sirro kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika kuweza kuhakikisha kwamba anaboresha huduma za kipolisi; na tumeona mara nyingi sana anafanya reshuffle za hapa na pale ili kuweza kuhakikisha kwamba ufanisi unaweza kupatikana katika jeshi la polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nichangie jambo moja la kitaifa zaidi, na hili ni jambo linalohusiana na mambo ya miundombinu ya Askari Polisi hasa katika vile vituo vya polisi vipo katika hali mbaya sana. Inasikitisha baadhi ya vituo vya polisi katika wilaya vinatia huruma. Kwa hiyo mimi nilikuwa naiomba tu Serikali na kuishauri Serikali tuweze kuhakikisha kwa namna moja ama nyingine tunakwenda kuboresha maeneo haya ili askari wetu waweze kufanya kazi katika mazingira yaliyokuwa salama zaidi.

Mheshimiwa Spika, la pili nilikuwa naomba nichangie katika eneo la kimkoa hasa katika mkoa wetu wa Pwani. Mkoa wetu wa Pwani ni Mkoa wa kimkakati tuna viwanda vingi sana, na kwatafsiri hiyo wawekezaji wapo wengi sana, lakini huduma za Jeshi la Polisi zinazopatikana hazikidhi haja, hasa katika suala zima la vifaa kama vile gari, gari za zimamotona hivyo kufanya askari wetu kupata tabu sana. Kwa hiyo ni vema Serikali waweze kuangalia katika eneo hili ili kuweza kuhakikisha Mkoa wa Pwani unapewa kipaumbele cha aina yake. Najua ni Tanzania kwa ujumla lakini Mkoa wa Pwani ni Mkoa wa Kimkakati kwa sababu kuna viwanda vingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho naomba nichangie kuhusiana na pale katika jimbo langu la Kibiti. Tunashida ya msingi sana pale katika Jimbo la Kibiti. Katika mwaka 2016 mpaka 2017 kulikuwa na hali mbaya sana ya mambo ya mauaji, na kwatafsiri hiyo Serikali iliweza kutoa tamko ikazungumza kwamba pale Kibiti itakuwa ni Mkoa Maalum wa Kipolisi. Kwa maana hiyo tunakwenda kujenga kituo cha kanda maalum ya kipolisi. Lakini mpaka hivi leo ninavyozungumza miaka takribani sita. Juzi wakati nikiwa nipo jimboni wazee wangu maarufu walinifuata, akiwemo mzee wangu maarufu sana anaitwa Mzee Saidi Lwambo, yeye aliniambia kuna ekari 25 zipo tayari tulizitenga miaka mitano iliyopita lakini mpaka leo Mbunge hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba tu niishauri Serikali; Kibiti tunahitaji tuwe na kituo cha Kanda Maalum ya Polisi kama tamko la Serikali lilivyokuwa linasema. Na huu ni ukweli ulio wazi kwa kuwa Afande Sirro akiwa anakuja kufanya mikutano katika Mkoa wa Pwani anakuja Kibiti na wanakuja askari wote wale, Ma-OCD wanakuja kutoka Kisarawe, kutoka Mkuranga, Kutoka Rufiji wengine kutoka Mafia wanakuja kukutana na Afande Sirro na mikutano inaendelea; na si mara moja wala mara mbili. Kwa tafsiri hiyohiyo Kibiti pale tupo katikati. Serikali ilivyoweza kutoa tamko kusema kwamba hapa ni kwenye kanda maalum ilikuwa ni maana halisi kwamba ni kanda maalum kwelikweli ukizingatia kwamba tumepoteza ndugu zetu wengi sana. Pale tupo katikati ya mkoa, kwa hiyo ni vema Serikali mzingatie suala la kujenga kituo hiki cha polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mimi nilikuwa naomba tu niseme, kwamba, katika majumuisho ya Mheshimiwa Waziri, na nipo serious katika jambo hili, nitashika Shilingi kama nisipoweza kupata tamko la Serikali kuhusiana na ujenzi wa kituo cha polisi cha Kanda Maalum katika Wilaya ya Kibiti; kwa sababu tumesubiri kwa muda mrefu sana na wananchi wa Kibiti wanahitaji huduma hizi.

Mheshimiwa Spika, Miundombinu iliyopo pale; tunazo eka 25 wananchi wameshazisafisha, zimekaa, kila miezi kila miaka wanasafisha maeneo yale lakini inashangaza Serikali tunashindwa basi hata kutenga cha kuanzia tu; japo milioni 300 au 400; kwamba hiki tunakitoa tunaenda kutengeneza kanda maalum. Kwa kufanya hivyo ni kwamba tunasuburi fedha nyingine zinakuja, lakini jitihada hizo hazijafanyika hata kidogo. Kwa hiyo nilikuwa naomba sana Serikali wahakikishe kuwa wanakuja na majibu ya msingi kuhusiana na suala zima la kanda maalum katika Wilaya ya Kibiti.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya kwa heshima na taadhima naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii nami kuwa mchangiaji siku ya leo. Awali ya yote, naomba nichukue fursa hii kukupa pole wewe pamoja na Bunge letu Tukufu kwa kuondokewa na mwenzetu, kipenzi chetu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia Muswada huu, naomba niseme neno moja tu kama siyo mawili. Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakati anaingia madarakani mwaka 2015, kauli yake kubwa sana ilikuwa ni kwamba yeye ndiye Rais wa wanyonge na hayo yamethibitika. Ameweza kulipigania hilo katika kuhakikisha mwananchi wa kawaida anakwenda kutetewa hali yake ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala zima la mambo ya kisheria sisi kama Wawakilishi wa Wananchi yanatukuta kule chini katika Mahakama za Mwanzo na Mahakama za Wilaya. Lugha inayotumika kule ni Kiingereza. Anakuja mwananchi ameshinda kesi, lakini hajui kama ameshinda kwa sababu lugha iliyokuwa imetumiwa mle ni “yes”, “no”. Kwa hiyo, hii inakuwa ni shida kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi niseme tu Muswada huu ulioletwa umeletwa hapa, namshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Vilevile nampongeza Waziri wa Katiba na Sheria pamoja na Mwenyekiti na timu yake nzima ya Kamati ya Sheria. Muswada huu ni sahihi, umekuja katika kipindi kinachofaa kabisa ili sisi Wawakilishi wa Wananchi twende kule chini tukawatetee wananchi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo, Kiswahili ni lugha ambayo inastahiki iendelee kutumika kwa sababu kubwa moja ya kulinda tamaduni zetu. Watoto wetu hawa sasa hivi wanaingia katika mitandao hii, kuna mambo mengi yanafanyika kule. Tutakapokuwa tunaitumia lugha yetu ya Kiswahili, ndiyo tutakapoweza kulinda tamaduni zetu hasa mambo haya ya kisasa; ndoa hizi za wenyewe kwa wenyewe, sijui rika moja, mwanaume kamuoa mwanaume, mwanamke inakuwa shida. Mambo haya yanarithiwa kwa sababu ya kutumia lugha za watu. Mheshimiwa Rais ameonyesha uzalendo na amepambana sasa hivi Kiswahili kinatumika kule SADC kama moja ya lugha ambayo inatumika katika mikutano yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tena nishukuru, lakini nimpongeze tena Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na Kamati yote kwa ujumla, kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuwa mchangiaji katika Wizara hii ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwanza kabisa nilikuwa naomba nichukue fursa hii kumpongeza kwa dhati ya moyo wangu Mheshimiwa Rais wetu ambaye ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Taifa, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya Tanzania hii katika sekta zote zile ikiwemo sekta hii ya maji vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Waislam tunaamini pale kwenye Quran kuna aya inasema kwamba wallahu yarzuku myashau bighairi hisab; kwamba Mwenyezi Mungu anamruzuku mwanadamu mambo bila hesabu ya aina yoyote ile. Sifa hizi zipo kwa mdogo wangu Aweso. Aweso ni mnyenyekevu, mtulivu, mwadilifu, mchapakazi, anaheshima, na mabega yake yapo chini kila siku. Ndugu yangu endelea kuwa hivyo hivyo chapa kazi na sisi kaka zako tuko nyuma yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, Mheshimiwa Waziri anamsemo wake huwa anasema, kwamba ukiona Kobe kapanda katika mti basi kapandishwa huyo si bure. Mimi niseme tu Naibu Waziri anafanya kazi kweli kweli. Nikushukuru sana dada yangu kwa kazi kubwa unayoifanya ya kuweza kumsaidia Mheshimiwa Waziri na kumsaidia Mheshimiwa Rais kwa kwa ujumla wake. (Makofi)

Mhehimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila; katika Wizara hii ya Maji kuna Katibu Mkuu ndugu yangu Sanga. Huyu bwana ni muadilifu kweli kweli huyu bwana ni muungwana kweli kweli anatoa ushirikiano kwa Wabunge ukimpigia simu anapokea pale ambapo akishindwa kupata simu yako anakutumia message na atakwambia samahani kiongozi nilikuwa kwenye mkutano. Katibu wetu Mkuu fanyakazi na mimi niseme tu katika kipindi hiki cha sasa hivi katika Awamu ya Sita Mheshimiwa Rais Wizara ya Maji inakwenda kufanya mabadiliko makubwa sana kwa kuwa na Katibu Mkuu kama ndugu yangu Sanga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee mbele. Mkurugenzi wetu wa RUWASA anafanya kazi nzuri kwelikweli, Mheshimiwa Rais akufanya kosa kuliona jicho lake pale lakini pale kwangu tuna meneja wa RUWASA, kijana yule anafanya kazi safi sana shida yake ni moja tu yule kijana ni Samaki Nchungu anatokea kule Mtwara na wale ni watoto wetu sasa tunashindwa kumpa zawadi pale Kibiti ya kuweza kumpa mke lakini anachapa kazi vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana nilisimama hapa, wakati nimesimama nilikuwa nimeomba fedha katika miradi mbalimbali ambayo iliyokuwa imesimama katika Jimbo la Kibiti. Mheshimiwa Waziri aliniambia kwamba kaka yangu usiwe na wasiwasi tutajitahidi kadri ya uwezo wetu tutapeleka maendeleo kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais. Mimi ninafaraja kusema tumepeleka fedha katika Mradi wa Mtunda Shilingi milioni 790 mkandarasi yupo site nani kama Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hivyo haitoshi tumeweza vile vile kupewa fedha pale katika Kata ya Mjawa Shilingi milioni 502 mkandarasi yuko site, mabomba yametambazwa katika Kata ya Mjawa utafikiri vile uyoga nani kama Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba niendelee mbele pale Kilula Tambwe kuna mradi mzuri sana wa maji umepelekwa pale shilingi milioni 452 mkandarasi yupo site kazi zinaendelea na Diwani wa Kata ile ndugu yangu Tabwe anaendelea kusimamia mradi ule safi sana Mheshimiwa Rais tunamshukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na yote hayo kuna mradi wa Shilingi bilioni 1.3 mradi wa pale Nyanjati kwenda kule Kivinja A. Mradi ule kila kitu kimeshakamilika tunasubiri tu kusaini makaratasi yale ya mkandarasi. Mimi nikuombe chondechonde Mheshimiwa Waziri hakikisha kwamba hili linaenda kufanikiwa na mwaka jana nilisema hapa mambo yakiwa mazuri tutakupa zawadi na kwa uadilifu uliokuwa nao jana niliwaona shemeji zangu sijui kama ile ruhusa umepata mke wa tatu yupo pale anakusubiri. Tunaomba sana tuhakikishe kwamba ule mradi unakwenda kusainiwa na unakwenda kufanya kazi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kubwa kuliko yote namshukuru sana Mheshimiwa Waziri. Nilimwambia kwamba katika Jimbo letu la Kibiti kuna maeneo ya Delta kule pamoja na kata za Kihongoloni, Maparoni, Mbuchi, na Msala. Tangu jimbo lile lilivyokuwa limeanzishwa hawajawahi kuona bomba, Mheshimiwa Waziri akaniambia kwamba bwana sikiliza tunakwenda kufanya mpango kutafuta fedha na tunaenda kufanya upembuzi yakinifu katika Bonde la Mto Rufiji. Nataka niseme tu, Mheshimiwa Waziri tunakushukuru sana mzigo umetoka shughuli zinaendelea piga kazi nani kama Mama Samia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa haya yanayotokea mimi niseme tu sisi watu wa Wilaya ya Kibiti tukiwa tunapigaga kura zile za kuchagua Rais ndiyo huwa tunaongoza Mkoa wa Pwani 2025 panapo uhai sijui Mama huyu atazibeba beba vipi zile kura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba niendelee mbele. Pamoja na kuyasema yote haya mazuri mimi nilikuwa naomba niishauri Serikali katika mambo mawili tu; jambo la kwanza nilikuwa naomba nishauri Serikali; jana nimewasikia Wabunge wenzangu na sisi ni wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania sizungumzii tu Kibiti peke yake tumesikia malalamiko ya watu kutoka Mtwara na watu kutoka Lindi, bajeti tunajua kwamba haitoshi, Mheshimiwa Waziri angalieni huko Serikalini kama itapendeza twende tukawatafute wadau ambao wanaweza waka-finance hii miradi na kuijenga vile vile wadau wapo mnaweza mkayatoa maji katika mradi ule wa Mtwara Ruvuma Walter Project wapo wadau wanaweza wakaifanya shughuli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama vile haitoshi, kwa ndugu yangu Mabula jana aliongea kwa ukubwa sana vile vile wadau wapo, tuwatafute ambao wanaweza wakaifanya miradi hii mikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine la msingi naomba niungane na Mheshimiwa Ngasa; jana alishauri jambo moja la msingi kwelikweli. Alisema kuwa kwenye hii miradi wakati tunatoa hizi tender tuangalie ukubwa wa zile tender. Najua kuna sheria zetu za manunuzi zinatubana, lakini tuwe flexible. Kama inapendeza kuna vimiradimiradi hivi milioni 500, milioni 700 labda mpaka bilioni moja itolewe katika ngazi ya wilaya kule tunaisimamia karibu sisi na madiwani na. Ile miradi mingine mikubwa mikubwa inaweza kwenda katika ngazi ya mkoa ili mambo mengine yakawa yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na yote haya, naomba tu niseme, Mkoa wetu wa Pwani mmetufanyia mambo makubwa sana ukizingatia kwamba pale sisi tumefungiwa mradi mzuri sana pale Chalinze kwa ndugu yangu Mheshimiwa Ridhiwani. Sisi Mkoa wa Pwani ni Mkoa wa Viwanda, maji ni uti wa uhai, lakini kama hivyo haitoshi katika shughuli zetu za mambo ya viwanda maji ni kitu cha msingi. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Rais, tunakushukuru sana Mheshimiwa Aweso piga kazi na sisi tupo atakayekuzingua na mimi nakwambia tu kaka zako tupo, tutakusimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la mwisho naomba nizungumze tena ni lamsingi kwelikweli. Mheshimiwa Waziri huyu ana mambo mengi. Sasa, ikikupendeza, tutakapopitisha hii bajeti mimi nilikuwa naomba tu unipe Mheshimiwa Naibu Waziri niende naye Kibiti, twende kule twende tukakague miradi ile, tukazungumze na wananchi kule. Nataka nimuhakikishie tu Mheshimiwa Naibu Waziri akifika kule pweza wataliwa kambare watapatikana changu wapo na mambo mengine yataendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na ninasema kwamba naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kuchangia kwenye bajeti ya Wizara yetu ya TAMISEMI. Niungane na wazungumzaji waliopita kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Mawaziri pamoja na Watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wanaifanya. Kubwa kuliko yote nimpongeze Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya, Watanzania wanajua, Afrika inafahamu na dunia vilevile inajua kazi anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa namna ya kipekee nimpongeze Mkuu wangu wa Mkoa Alhaji Abubakar Kunenge, baba huyu ni mchapa kazi, anasimamia vizuri shughuli za kimaendeleo katika Mkoa wetu nasi tunafarijika sana na uwepo wake katika Mkoa wetu wa Pwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijachangia bajeti hii naomba nikumbushe mambo mawili, matatu ambayo yapo katika Jimbo letu la Kibiti. Jambo la kwanza naomba nikumbushe ahadi ambazo zimetolewa na Wizara hii katika miaka miwili iliyopita. Kuna ahadi ya ujenzi wa barabara katika kiwango cha lami kutoka pale Kibiti Mjini kwenda katika jengo letu la Halmashauri. Wizara hii ilitoa ahadi mpaka sasa hivi bado haijatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii katika suala zima la ujenzi wa kituo cha afya. Tuna fedha ambazo tulikuwa tumeziomba na zilizokuwa zimeahidiwa shilingi milioni 200 katika kituo chetu cha afya cha pale Bungu ili tuweze kukamilisha baadhi ya majengo. Fedha hizo hazijatoka nasi tunazihitaji, Mheshimiwa Waziri nakujua upendo ulionao, najua tu kwamba hizi fedha unaenda kuzitoa ili sasa tuweze kuona jinsi gani wananchi wa Bungu katika Jimbo la Kibiti wanaenda kunufaika na uwepo wako katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Salale katika eneo la Nyamisati. Mheshimiwa Waziri eneo lile lina watu wengi sana, tunahudumia vilevile Wilaya ya Mafia, kuna zahanati iliyopo pale lakini zahanati ile imehewa. Tuna shule iko pale ya Sekondari ya WAMA wananchi wako wengi, ndugu zetu kutoka Mafia wanategemea pale, chondechonde tunaomba sana tuweze kukamilishiwa ili tuweze kujenga katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, wiki mbili zilizopita tulikuwa na Azimio hapa la kuweza kumpongeza Mheshimiwa Rais, moja katika nukta ambayo tulikuwa tumezungumza ni suala zima la kudumisha demokrasia. Mimi niseme tu tuende mbali zaidi, pamoja na pongezi hizo Mheshimiwa Rais vilevile tunapaswa tumpongeze jinsi alivyoweza kudumisha suala zima la uzalendo katika nafsi za Watanzania.

Mheshimiwa Spika, ninayasema haya kwa sababu ninapenda kutumia nafasi hii kumpongeza sana Mwenyekiti wangu wa Kamati ya LAAC Mheshimiwa Halima James Mdee, kwa uzalendo wake mkubwa anaouonesha, tumeweza kufanya nae kazi katika kipindi kifupi lakini huko tulikokuwa tunapita katika ziara zetu unaona jinsi gani alivyokuwa anaweza kuwatetea Watanzania. Fedha za Serikali zinavyokuwa zinapotea na yeye jinsi alivyokuwa anatoa mapovu katika kuweza kuzisemea. Katika hili sina shaka, Mheshimiwa Halima James Mdee uzalendo wake hauna kiwango ni lazima uweze kuigwa na Wabunge wengine wote waliopo humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie bajeti hii katika nukta zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichangie katika suala zima la asilimia 10. Serikali mmekuja na maelezo mazuri sana na kuweza kusisitiza suala zima la asilimia kwamba sasa hivi limesitishwa kwa muda, lakini hivyo haitoshi! Ningependa sana Mheshimiwa Waziri wakati unakuja kuhitimisha hapa utueleze zile fedha zilizopotea kule chini kwenye Halmashauri Serikali mna mpango gani wa kuweza kuzirudisha fedha hizo. Hili ni jambo la msingi sana kwa sababu fedha nyingi zimepotea na wale wanaoitwa Maafisa Masuuli they are not accountable katika suala hili.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la msingi ambalo vilevile Mheshimiwa Waziri naomba nilisisitize ni kuhusiana na suala zima la uhamisho wa watumishi. Pamekuwa na destruri mbaya sana katika Wizara ya TAMISEMI. Mtumishi anafanya maovu katika taasisi moja au katika Halmashauri moja lakini kinachotokea anakwenda kuhamishwa kwenda katika Halmashauri nyingine, hiki kitu hakikubaliki. Mamlaka ya nidhamu lazima ichukue nafasi yake hivi sasa kuweza kuhakikisha watumishi wote ambao wanakuwa wanafanya madhambi katika Halmashauri sio tu kwamba wanahamishwa kwenda katika eneo lingine, vilevile wanakwenda kuchukuliwa hatua za kinidhamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la mwisho na la msingi sana ambalo nataka nilisisitize ni kuhusiana na suala zima la mambo ya ajira. Zimetangazwa ajira na mimi niseme tu katika Jimbo langu la Kibiti tuna shida kubwa sana katika suala zima la Walimu. Mimi nina Walimu wanaojitolea hivi sasa takribani zaidi ya 100, katika eneo la sekondari nina Walimu wasiopungua 60, katika eneo la msingi nina Walimu wanaojitolea wasiopungua 81 na katika sekta ya afya kuna watumishi wasiopungua 45. Mimi niseme kupanga ni kuchagua.

Mheshimiwa Spika, kuna baadhi ya watumishi ambao wamekuwa wakiomba ajira hizi, kinachokuwa kinafanyika wanatumia Wilaya hizi ambazo ziko pembezoni kama madaraja, wakishafika kule kinachofuata wanasema kwamba mazingira siyo rafiki, mwingine anasema hali ya hewa siyo nzuri, mwingine anaongopa sijui leo nimelala, kesho nimeamka niko nje, mwengine anaongopa fedha zangu zimeibiwa katika mazingira ya kutatanisha, hii kitu haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni lazima sasa kama Serikali mje na mkakati halisia Walimu hawa wanaojitolea waweze kupewa kipaumbele ili sasa tuweza kuona ni jinsi gani kwa namna moja ama nyingine wanakwenda kutusaidia katika maeneo yetu. Kuna
vijana wengi sana ambao wanayajua mazingira haya lakini vijana hawa kimbilio lao kubwa sana ni kwa Wabunge na Wabunge wengi wamesimama humu ndani wanalisisitiza jambo hili, ni lazima sasa ifike wakati Serikali mje kuwa na maamuzi halisia.

Mheshimiwa Spika, haiwezekani watu wanajitolea lakini Serikali inakwenda kutoa ajira kwa watu wengine, sawa wote ni Watanzania lakini hawa wanaojitolea nao wanazo sifa, ndiyo maana wanafunzi wanafaulu. Sasa kama hivyo ndivyo lazima sasa muweze kuhakikisha mnakuja na jambo halisia la kuweza kuajiri vijana hawa ili waweze kupata ajira.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami kuweza kuchangia katika Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze tu kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa hili. Sambamba na hilo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuweza kuwapa dhamana wadogo zangu Mheshimiwa Bashe pamoja na Ndugu yangu ili kuweza kuiendeleza Wizara hii, kiukweli wamekusudia kuweza kutengeneza legacy ya aina yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kiongozi mzuri ni yule ambaye anao uwezo wa kuchukua maamuzi na kuyasimamia maamuzi hayo. Nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Bashe, pale kwetu katika Mkoa wa Pwani tulikuwa na mfanyabiashara ya uchuuzi wa kukamua mafuta lakini kwa bahati mbaya hakufuata taratibu husika ikiwemo kupata leseni za kibiashara, vyombo vya usalama vilimkamata lakini nikushukuru sana Mheshimiwa Bashe ulichukua maamuzi magumu na uliweza kusimama katika maamuzi yale, ulisema kwamba asaidiwe mtu yule ili aweze kufanyiwa registration na process zingine zote hivi ninavyozungumza umefanya multiply effect ya hali ya juu, mtu yule sasa hivi anaichangia Serikali kwa kulipa kodi, safi sana endelea Ndugu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najivunia kuwa na Rais Samia kama Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Rais Samia kuwa kama Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi Taifa, pia najivunia vilevile Chama cha Mapinduzi kuwa ndiyo Chama kilichotengeneza dola. Kuna sifa nyingi sana lakini nitagusia sifa moja Serikali hii ni Serikali sikivu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilisimama hapa mwaka jana, nilileta kilio cha watu wa Jimbo la Kibiti wakiwa wanalalamika katika mambo makubwa mawili, jambo la kwanza ilikuwa ni suala zima la bei ya korosho na ufuta lakini jambo la pili ilikuwa ni suala zima la tarehe za kufanyika minada. Wale Ndugu zangu Wamakonde kule Mtwara na pale katikati Lindi walikuwa wanafanya minada tofauti nasi huku Baba zao watu wa Rufiki, hii ilikuwa inapelekea wakulima wetu kuuza mazao kwa bei ya chini, nilivyoleta kilio hicho nakushukuru sana Mheshimiwa Bashe na Serikali hii ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana bei ya juu ya ufuta iliuzwa shilingi 2,556 katika Mkoa wa Pwani, kama hiyo haitoshi bei ya korosho iliuzwa shilingi 2,155 tunakushukuru sana na tunamshukuru Mheshimiwa Mama yetu Samia Suluhu Hassan. Pia ninamshukuru sana Mheshimiwa Mkuu wangu wa Mkoa Alhaji Abubakar Kunenge, Baba yule anafanyakazi kwelikweli, alihakikisha anafanya transformation katika masuala mazima ya kilimo ndani ya Mkoa wetu wa Pwani. Namshukuru sana Mkuu wangu wa Mkoa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo makubwa mawili tu ya kushauri kwa Serikali, jambo la kwanza hili Bonde la Mto Rufiji kule ambako kuna ule mradi wanasema Rufiji Hydroelectric Power kuna upstream na downstream, sisi tupo kule downstream Wandengereko watu wa Rufiji, watu wa Kibiti pamoja na watu wa Mkuranga, ninaishauri Serikali tuweze kuangalia uwezekano wa kufanya kilimo cha umwagiliaji, nililisema hili mwaka jana lakini ninakuamini Mheshimiwa Bashe utalichukua na utakwenda kulifanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka niishauri Serikali ni kwamba katika taratibu zetu za kufanya mambo ya mauzo ya korosho na ufuta kuna kitu kinaitwa Fomu Na. Saba.

Mheshimiwa Bashe niliwahi kukufuata katika jambo hili, tunapozungumzia suala zima la Fomu Namba Saba ni pale ambapo wale venders wanaonunua ufuta ama korosho wakiwa wanalipia kama tani 500, wanapokwenda katika ghala wanakuta tani 200, kwa tafsiri hiyohiyo makampuni ya insurance yanakuwa yanahusika kuweza kuwalipa. Mwaka jana 2021/2022 fedha ambazo mpaka hivi sasa zipo kule katika Bodi ya Maghala tunazungumzia bilioni 1.4. katika fedha hizi shilingi milioni 600 tu ndiyo zimelipwa. Kuna baadhi ya makampuni ya insurance hayalipi malipo hayo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na Kanuni zetu za Kibunge naomba niyahifadhi makampuni hayo lakini Mheshimiwa Bashe nitakufuata nikwambie makampuni gani yanayotuangushwa. Hawa venders ndiyo wadau wetu wakubwa wa maendeleo, tunategemea kwa kiasi kikubwa sana tunapokuwa tuna shughuli mbalimbali za kimaendeleo wao ndiyo wanakuja kutuchangia, pale ambapo wananunua mazao halafu mazao yale hawayapati na pale ambapo panakuwa panatokea upungufu halafu hawalipi kwa wakati hii inawakatisha tamaa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante.

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia kwenye hii Finance Bill. Kabla sijaanza kuchangia, nilikuwa naomba tu nichangie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa bajeti ambayo jana tumeipitisha kihistoria kabisa.

Vilevile, niwapongeze Mawaziri; Waziri wa Fedha pamoja na Naibu wake, nawapongeza pia Wabunge wenzangu ambao wapo katika Kamati ya Bajeti kwa kazi kubwa na nzuri ambayo wameweza kuifanya katika kumsaidia Mheshimiwa Waziri katika kuhakikisha kwamba bajeti hii inapitishwa ipasavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina nukta nne tu za kuchangia katika hii Finance Bill. Nukta ya kwanza yenyewe inahusiana na suala zima la tozo la asilimia 10 kwa zile motorcycle zinazoingizwa zenye umri zaidi ya miaka mitatu. Tukiangalia katika hii Finance Bill, hii Amendment of the Excise and Management and Tariff ipo kwenye Cap. 147, yenyewe inazungumzia kwamba kutakuwa na tozo ya asilimia 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni suala la busara, lakini nami nilikuwa naomba kidogo nikazie hapa. Tafsiri yake pana ni kwamba, tunakwenda kuvilinda viwanda vyetu vya ndani. Nami nizungumze Kitaifa, lakini vilevile kwa interest kubwa sana ya Mkoa wa Pwani ambapo kuna viwanda vingi sana vina assemble pikipiki hizi. Nafikiri hii tozo ya asilimia 10 ingeongezwa kidogo, ingeenda mpaka asilimia 20. Kwa sababu, tafsiri halisi ni kwamba unapozungumzia life span ya motorcycle, haiwezi ikazidi miaka mitano. Kwa sababu mtu anaitoa pikipiki kutoka huko, anaileta hapo, tutakuwa tunawa-discourage sana wale wawekezaji ambao tunao tayari ndani ya nchi na hii itakwenda kuathiri sana katika zile kodi ambazo, tunakusudia kuzikusanya sisi kama Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa nashauri, ikiwezekana basi Mheshimiwa Waziri liangalieni hilo, wakati mnakuja kufanya majumuisho ikiwapendeza hii asilimia 10 twende juu kidogo, maana yake hapa tunajaribu ku-discourage kufanya nchi yetu kuwa kama ni dumping. Kwa hiyo, twende katika asilimia 20 ili tufanye total discouragement ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ambalo nilikuwa naomba nilichangie, hili ni kuhusiana na suala zima la mabadiliko pale PTA. Hii ipo katika ukurasa wa 17, tunapojaribu kuangalia suala zima la Amendment of the Ports Act na hii inajumuisha vile vile, katika ukurasa wa 33 na ukurasa wa 34 tunapoigusa TASAC na wakati huo huo tunapoigusa TCRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokifanya, tunakwenda kuchukua mapato yote yale yanapelekwa kwenye account maalum ambayo itaenda kufunguliwa pale Benki Kuu. Sasa mimi sielewi na sijui kama hii ndiyo ile inayoitwa Treasurer Single Accounting System au ni kitu kingine kidogo kipo tofauti. Kwa sababu tunachokifanya hapa, tusipokuwa makini sana kama Serikali, maeneo haya yako very strategic. Unapozungumzia TPA, ipo very strategic katika masuala ya kiuchumi. Unavyozungumzia suala zima la TASAC, ni very strategic vile vile katika masuala mazima ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hivyo haitoshi, mpaka TCRA tumeona hapa, tumeweza kuwekeza tozo zile tunazoenda kuzikusanya zitakazoweza kutusaidia ili tuweze kwenda kufanya shughuli za kimaendeleo kwenye maeneo mengine. Sasa, tunavyoweza kwenda kuziweka zile fedha pale, Pay Master General ndio anakwenda kule ku-approve zile expenditure.

Mimi naona hii tunaenda kuweka unnecessary bureaucracy. Kwa hiyo, nafikiria ikipendeza, tuache tu system iendelee. Unajua Waingereza wana msemo wao, wanasema: “don’t fix it if it is not broken.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mazingira yalikuwa yanaendelea kama kawaida, why do we need to fix it again? Tuache tu ili sasa tuweze kuona, taasisi hizi zinakwenda kufanya kazi kama ipasavyo. Tusipokuwa makini Serikali tunaweza tukaenda ku-paralyze taasisi hizi. Kama yale yaliyokuwa yameshatokea kule TANAPA, mazingira yalikuwa siyo rafiki mpaka Serikali ikaamua kuingia kati na kuanza kupeleka mashambulizi ya fedha kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kuna solution mliyokuja nayo ambayo inasema kwamba mnakwenda kupeleka fedha za OC za miezi miwili, lakini tujue tu, hizi taasisi ziko very sensitive. Kuna mambo ambayo yanapaswa yafanyike kwa haraka haraka, sasa decision making processes zetu kidogo zinaweza zikawa zina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokuwa nafikiria ambacho mnapaswa mkifanye ni kwenda kufanya proper control katika taasisi hizi rather than kwenda tena katika mfumo, kule katika Central Bank, kufungua akaunti, fedha zikaenda kule, wale wakiwa wanahitaji fedha, sasa wafanye request. It makes no any difference kama vile wanavyofanya kule katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo katika Halmashauri huwa hayaendi kwa wakati kwa sababu ya hizi bureaucracy hapa katikati. Makaratasi yanakusanywa pamoja, sijui yanapelekwa Benki Kuu yawe authorized, halafu ndiyo malipo yaweze kufanyika. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri eneo hilo tuweze kuliangalia kwa karibu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilikuwa naomba nilichangie ni eneo linalohusiana na masuala mazima ya malipo. Hapa tunakwenda kufanya amendment inayohusiana na Amendment of the National Payment System Acts. Hii amendment tunayoenda kuifanya, tunaipa mamlaka sekta husika au Wizara husika kwamba sasa wanakwenda kutengeneza regulation ili sasa ziweze kutumika ili tuone ni jinsi gani yale makato ya simu yanayoenda kufanyika kule yaweze kwenda kama ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nitoe tahadhari hapa. Sisi tunayo hapa Kamati ya Sheria Ndogo, nafikiri ingekuwa ni busara zaidi, hizi kanuni ambazo zinakwenda kuandaliwa sasa na Wizara, kabla hazijaenda kuwa implemented ziletwe hapa Bungeni. Tunaye Mwenyekiti wa Kamati ya Sheria Ndogo, ana umahiri mkubwa sana na Wabunge wenzetu. Ziletwe zile kanuni wazipitie. Watakapoweza kujiridhisha, basi tafsiri yake ni kwamba tunakwenda kuzi-implement. Kinyume na hapo nachelea kusema kwamba, yasije yakatokea kama yale yaliyotokea kwenye vikokotoo. Hii nafikiri inaweza ikawa ni tafsiri pana sana na hii tusipokuwa makini linaweza likawa ni tatizo la msingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana, niweze kuchangia katika eneo hilo, tuweze kuona tunavyoenda kumpa freedom moja kwa moja Waziri husika na taasisi ile kwenda kuandaa kanuni zile, hii inaweza ikaja ikaleta shida. Lazima hizo kanuni zije Bungeni, wale watu wa Kamati ya Sheria Ndogo wapo, wazipitie. Wao kwa niaba yetu watakapoweza kuzi-authorize zile, basi ziweze kutumika. Hii tunaweza tukaenda kuchukua control measure ya hali ya juu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nilikuwa naomba vile vile nilichangie, ni kuhusiana na hii amendment ambayo ilikuwa imeenda kufanyika, Amendment of the Road and Fuel Tolls Act, tumeenda kuongeza shilingi moja kule. Hili ni jambo la busara sana. Naipongeza sana Serikali, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri pamoja na wataalam wake kwa ujumla wao kwa kuweza kuja na ubunifu wa hali ya juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo nachelea kusema kitu kimoja tu, sijaona hapa, labda Mzee Mpembenwe wakati ananipeleka shule, hii lugha ni ya wenzetu labda sielewi vizuri. Sijaona kama hizi fedha zinazoenda kupelekwa kule katika huo mfuko zimeenda kuzungushiwa ili sasa kuweza kuwa na uhalisia kwamba zinakwenda moja kwa moja kwenye Mfuko ule wa TARURA tunaokusudia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nilikuwa naomba sana, labda kama ni tatizo la lugha, naomba tu ieleweke hivyo, basi Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha atatuambia. Kinyume na hapo, kutokana na tafsiri ya maelezo haya ambayo yamezungumzwa hapa, sijaona kama kuna kipengele kinachosema kwamba fedha hizo zitakuwa per-se kwa ajili ya suala zima la TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema haya, kwa heshima na taadhima naomba kuunga mkono hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)