Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Josephat Mathias Gwajima (24 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa dakika chache hizi za kuchangia na mimi katika hotuba ya Rais ya kufunga Bunge na hotuba ya kufungua Bunge la Kumi na Mbili.

Mheshimiwa Spika, kila mara ninapomkumbuka Dkt. John Pombe Magufuli na hotuba zake na uongozi wake inanikumbusha kitabu kimoja kilichoandikwa na Dkt. John C. Maxwell. Kwenye kitabu chake anasema; ikitokea vita kati ya kundi hili na kundi lile au kati ya nchi hii na nchi ile na ikatokea kwamba jeshi moja wanajeshi wake wote ni simba na kiongozi wake ni simba na jeshi lingine wanajeshi wake wote ni kondoo na kiongozi wake ni simba, basi hizi timu mbili zikipigana kwa maana ya timu ambayo kiongozi ni simba na askari ni simba na timu ambayo kiongozi ni kondoo na askari ni simba, definitely timu ambayo kiongozi ni kondoo itapoteza vibaya sana. (Makofi)

Lakini pia Maxwell akasema kwamba; pamoja na kwamba jeshi linaweza kuwa na masimba wote ilimradi tu kiongozi ni kondoo, lazima jeshi hilo litapoteza; alikuwa anaongea kwa habari ya dhana ya uongozi, kwamba maendeleo au ushindi ni kiongozi. Kwa bahati nzuri Tanzania tumepata kiongozi Simba na majeshi nayo ni simba na kwa hakika ushindi wetu upo kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ninapokumbuka dhana ya uongozi wa kidiplomasia, ninakumbuka mambo mawili; kwenye diplomasia, uchumi wa kidiplomasia tuna mambo mawili; tuna uchumi pamoja na biashara, lakini kwenye diplomasia ya uongozi tuna mambo matatu; cha kwanza tunasema strong power, cha pili soft power na cha tatu smart power.

Mheshimiwa Spika, sasa strong power ni nini; strong power ni mahali ambapo kiongozi anashawishika kwamba watu wangu nikiwapeleka mpaka pale wantanufaika na maisha yao na maisha yao yatakuwa salama. Lakini watu wale ama kwa kujua au kwa kutokujua hawajui kwamba wakifika pale watakuwa salama. Sasa strong power maana yake ni kiongozi huyu anawakokota hawa watu wapende wasipende wakifika pale wakagundua faida zake wanamshukuru yule kiongozi wanasema ahsante kwa kutufikisha hapa, hiyo inaitwa strong power.

Mheshimiwa Spika, soft power ni kwamba unaanza kuwabembelezabembeleza, unawaeleza faida za wanakokwenda, watakakofika na mambo ambayo watayapata, unawabembelezabembeleza mpaka unawafikisha pale baadaye wanakushukuru wanasema ahsante kwa kutufikisha hapa, hiyo inaitwa soft power.

Mheshimiwa Spika, lakini smart power unaunganisha strong power pamoja na soft power; kuna wakati mwingine unawaburuza wanakwenda, kuna wakati mwingine unawabembeleza na hiyo ndiyo aina ya uongozi ambayo Dkt. John Pombe Magufuli anayo. Dkt. John Pombe Magufuli ni smart power na Mawaziri wetu na Waziri Mkuu pia ni smart power, watatufikisha tunakotakiwa kwenda kwa uhakika kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, TARURA; hai-make sense ukiona kwamba mtandao wa barabara za TARURA ni takribani kilometa 130,000 na mtandao wa barabara za TANROADS ni takribani kilometa 40,000, hai-make sense kwa nini mpaka leo TARURA anapewa asilimia 30 na TANROADS anapewa asilimia 70; hai-make sense. (Makofi)

Nikisema hivyo sina maana kwamba nadharau ukweli wa kwamba ubora wa barabara za TANROADS unatakiwa kuwa imara zaidi kwa sababu una-cut accross mikoa kwa mikoa, lakini hai-make sense kwa nini huyu ambaye ana mtandao wa kilometa 130,000 apewe asilimia 30 na huyu mwenye mtandao wa kilometa 40,000 apewe mgao wa asilimia 70; hakuna mateso tuliyonayo Wabunge kama TARURA kukosa fedha kule mikoani, ni ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano kwenye Jimbo langu la Kawe. Kwenye Jimbo la Kawe Wilaya nzima ya Kinondoni tuna kilometa za barabara za ndani 1,663. Kilometa 200 ziko Jimbo la Kinondoni kwa pacha wangu Mheshimiwa Tarimba, lakini kilometa 1,463 ziko Jimbo la Kawe; kilometa I,463, ni sawasawa na kutoka Dar es Salaam mpaka Kigoma lakini zote ziko ndani ya Jimbo la Kawe. Nilipowatembelea TARURA wana fedha za kutengeneza kilometa 120. Ina maana kuna kilometa 1,300 ambazo haziwezi kutengenezwa, this is not acceptable kwa wakati wowote katika nchi yetu; haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kama kweli tuna ndoto ya kuwaletea watu maendeleo, siyo Jimbo la Kawe tu, lakini kwenye kila jimbo barabara zinazotakiwa kujengwa kwa kutumia fund ya TARURA hazitajengwa kabisa kama TARURA hataongezewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Road Fund kama unavyojua ni mawazo yaliyoanza mwaka 1999 mpaka 2000 nyakati zile Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa Waziri wa Ujenzi. Kuanza kuchukua shilingi 200 kwenye kila lita moja ya mafuta na kuchukua asilimia 70 kwenda TANROADS na asilimia 30 kwenda TARURA.

Ninawaomba watendaji wawaze mawazo mengine tena ya kuongezea fedha. wasitegemee mawazo yaleyale ya Dkt. John Pombe Magufuli alipokuwa Waziri wa Ujenzi, wawaze mawazo mengine ya kuongezea fedha. There is nobody here who is a copy of the other, everybody is an original from the Almighty God; lazima watendaji kazi wetu mjiongezee zaidi, muwaze zaidi, muwe creative zaidi kwa namna ya kumuongezea TARURA fedha, vinginevyo it is a nightmare kuwapa watu maendeleo kwa kupitia TARURA. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna huyu mdudu anaitwa Corona…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana, dakika tano zimekwisha. (Makofi/Kicheko)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pasipo kifani kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia kwenye Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao umewakilishwa na Waziri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa mama Kilango Malecela leo alikuwa anachangia nikamwomba aniazime dakika zake tano na akakubali. Sasa kama wewe itakupendeza basi niunganishe dakika tano za Mheshimiwa mama Malecela na za kwangu nipate dakika kumi ili niweze kutoa nilichonacho. Nimezungumza naye akasema anachangia na akaniruhusu lakini nikasema nikipata ruhusa yako na hekima yako itapendeza sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Gwajima, hiyo hairusiwi, Wabunge huwa hawapeani muda lakini muda wako sasa unazidi kwenda kwa hayo maombi ambayo yamechukua muda kidogo, tafadhali anza kuchangia. (Makofi/Kicheko)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maneno machache sana kwa sababu ya muda wangu, kuna hoja zinazungumzwa hapa kuonyesha kana kwamba awamu ya Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli haijafanya jambo lolote. Mtu yeyote ambaye haoni kwamba miaka mitano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli haijafanya chochote basi anaweza kuwa na ugonjwa hatari sana ambao hauwezi kutibika hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua fika kwamba kuanzia mwaka 1976 mpaka 1981, Tanzania ilikuwa na ndege almost 11 na mpaka tunafika kwenye ubinafsishaji tulikuwa na ndege 9 na mpaka Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli anaingia madarakani tukawa hatuna ndege. Hata hivyo, tangu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameingia madarakani tuna ndege zinaelekea 12 sasa. Asiyeona hayo ana ugonjwa special unahitaji daktari special. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini unakumbuka vizuri Shirika la TANESCO, kabla ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hajaingia madarakani lilikuwa linaendeshwa kwa kupewa ruzuku shilingi bilioni 438 kila mwaka, lakini tangu 2015 Shirika la TANESCO linajiendesha kwa fedha yake lenyewe na linafanya vizuri sana. Asiyeona ana ugonjwa maalum unahitaji daktari maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hivyo tu, mwaka 2015 Tanzania yote ilikuwa na vijiji 2,018 vilivyokuwa na umeme lakini leo ndani ya miaka mitano vijiji 10,263 vina umeme katika nchi ya Tanzania. Kwa taarifa ya asiyeona ni kwamba vimebaki vijiji 2,005 tu Tanzania yote iwe na umeme. Pamoja na mambo mengine yote lakini mwenye macho ni muhimu aone kitu gani kimefanyika na wapi tunaelekea kwa sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna watu wanasema msiongelee sana Stigler’s Gorge ni ileile, sikiliza nikwambie tangu Tanzania ianze ina megawatt za umeme 1,602, hii ni tangu Mwalimu Nyerere, Mheshimiwa Mwinyi, Mheshimiwa Mkapa na Mheshimiwa JK Kikwete, utaachaje kuongelea Stigler’s Gorge ambao ni mradi mmoja wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ambao umetupa megawatt 2,115. Lazima akili iwe likizo au ina matatizo maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hebu tuseme ukweli, mimi nimekuwa Japan, wao wana treni inakwenda kwa speed 250 na wana nyingine ambayo watazindua mwaka ujao inayotembea chini ya ardhi inayokwenda kilomita 500 kwa saa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Tanzania kwa Afrika Mashariki tumekuwa nchi ya kwanza kutekeleza mradi wa treni yenye uwezo wa kwenda kilomita 160 kwa saa. Utasemaje Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hajafanya vitu vyake? Unahitaji dawa maalum na daktari maalum kusema hivyo. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haitoshi, hebu tuangalie ukweli, wakati Mheshimiwa Dkt. Pombe Magufuli anaingia madarakani tunaambiwa tembo wa Tanzania walikuwa wamebaki 15,000, leo kwa taarifa ya Wizara ya Maliasili tuna tembo 60,000. Kwa utawala wa Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli mpaka tembo wanaanza kuzaana bila utaratibu. Huwezi kusema Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli hajafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa mfano afya, nagusia kila mahali kwa sababu muda wangu haunitoshi, tangu Uhuru tumekuwa na Hospitali za Wilaya 77 lakini miaka mitano ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tumejenga Hospitali zingine za Wilaya 102. Utabezaje hizo juhudi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini haraka haraka tulikuwa na Hospitali za Rufaa za Mikoa 18 tu tangu Uhuru ndani ya miaka tano zimejengwa mpya 10. Asiyeona ana ugonjwa unaitwa Schizophrenia.

T A A R I F A

MWENYEKITI: Mheshimiwa Gwajima, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namsubiri. (Kicheko)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Napenda tu nimpe taarifa anayenisubiri, kwanza hapa tunachangia Mpango kushauri Serikali, tunavyosema Mpango haujatekelezeka hatumaanishi kwamba Mheshimiwa Dkt. Magufuli wa Awamu ya Tano hajafanya kitu. Mfano kwenye umeme alipotaja target tuliyojiwekea mpaka 2021 ilikuwa tufikie megawatt 4,915 lakini mpaka sasa hivi tuna megawatt 1,601 wakati mwaka 2014/2015 ilikuwa ni megawatt 1,501. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukisema kwamba wanaweka target na hazifikiwi siyo kwamba tunasema hakijafanyika kitu lakini wanavyoweka viashiria basi viweze kufikiwa angalua kwa asilimia 80. Asipambe bali ashauri ili Serikali ifanyie kazi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Esther Matiko. Mheshimiwa kabla sijakuuliza kama unapokea taarifa, nadhani tuwe tunaelewana vizuri, mtu anayegoma kutambua kilichofanyika na mtu anayetambua kilichofanyika lakini anatoa ushauri wa nini kifanyike zaidi kuna tofauti kati ya hayo mambo mawili. Mheshimiwa Gwajima unapokea taarifa hiyo? (Makofi)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nimwambie msomi yeyote kabla hajaenda mbele ana-refer kwanza kule alipotoka. Mimi nime- refer kwanza alipotoka Mheshimiwa Dkt. Magufuli na Mpango uliowekwa na Waziri wa Magufuli Mheshimiwa Dkt. Mpango wa kule tunapoelekea. Kwa hiyo, taarifa yake haina maana yoyote kwangu, naomba niendele Mheshimiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye vituo vya afya tangu Uhuru tulikuwa na vituo vya afya 535 lakini ndani ya miaka mitano tumejenga vituo vya afya 487. Kama hiyo haitoshi tangu uhuru tulikuwa na zahanati 4,554 lakini ndani ya miaka mitano tumejenga zahanati mpya 1,998.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme jambo moja kwamba haya yote niliyoyasema hayamaanishi kwamba tusitekeleze Mpango mpya uliowekwa mbele yetu. Nataka kila mtu afahamu kuna ugonjwa wa COVID-19 ambao ni ugonjwa umetikisa dunia na nchi yetu imechukuwa msimamo tofauti na nchi nyingine zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge nataka kutumia nafasi hii kuwatia moyo; msiogope. Msiogope mnapoambiwa kwamba kuna phase ya pili ya COVID-19. Kilicho na nguvu nyuma ya COVID-19 ni woga uliotengenezwa juu ya COVID-19; the fear over COVID-19 is even more powerful than COVID-19 itself.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wote na watu wote tushinde woga, tusiogope, tumeshinda, tusonge mbele. Msimamo wetu wa kutokuchanjwa na msimamo wetu wa kutokufanya social distancing ni msimamo sahihi na utatufikisha mahali sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha mwisho, watu wengi wanazungumza kusahau tulikotoka wakifikiri historia when you don’t remember where you are coming from, you are bound to make mistakes where you are going thinking you are doing development, but you may do the same because you don’t know where you are coming from.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu kule nyuma ilikuwa na miradi ya wachimba madini. Tulikuwa tunapewa royalties peke yake, nchi yetu ilikuwa inapata royalties peke yake ya makampuni ya madini. Sasa hivi Mheshimiwa Rais amesukuma tunapata almost asilimia 50 na Tanzania ni wamiliki wenza wa madini yanayochimbwa na kampuni za madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nikushukuru sana kwa kunipa muda ili niweze kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuwaambia ndugu zangu Waislamu wa Jimbo la Kawe na Waislam wote wa Tanzania nzima kwamba Ramadhan Kareem na Ramadhan Mubarak. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa makusudi ya kuokoa muda, napenda kumpongeza Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuapishwa kuwa Rais wa Sita wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Pia nampa pole kwa kuondokewa na aliyekuwa Rais wake ambaye pia ni Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Amiri Jeshi Mkuu wa Majeshi ya Tanzania Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hapo, naomba uniruhusu kwa sababu huu ni mwezi Mtukufu wa Ramadhan, nianze hotuba yangu kwa kunukuu andiko moja kwenye Maandiko Matakatifu. Kitabu cha Hosea 4:6 inasema hivi: “Watu wangu wanaangamia kwa kukosa maarifa”. The English version says: “My people are destroyed for lack of knowledge”. Pia andiko hilo hilo limeandikwa kwenye Kitabu cha Methali 29:18. Kitabu hiki kiliandikwa na Suleiman Bin Daudi, Mfalme aliyewahi kuishi miaka mingi iliyopita, alisema hivi: “Watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa maono”. Kiingereza chake, anasema: “My people are destroyed for lack of vision”. Kwa hiyo, tunapata ujumla kukosa maono kunaangamiza na kukosa maarifa kunaangamiza; lack of vision destroys and lack of knowledge as well as destroys.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini sasa nimesema hayo? Kwa sababu nimekuwa nikijiuliza sana, kwa nini nchi zetu za Kiafrika na Taifa letu likiwemo, haziendi kwa speed ya maendeleo kama inavyotakikana. Ukiangalia resources ambazo zimo ndani ya Bara la Afrika na nchi yetu, hazihusiani na speed ya maendeleo ambayo Waafrika na Watanzania tuko nayo. Kwa nini? Nimekuwa nikiangalia, kwa mfano, asilimia 91 ya reserve ya almasi duniani inatokea Bara la Afrika; na asilimia 64 ya dhahabu duniani inatokea Bara la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, haitoshi, kwenye nchi yetu tuna dhahabu, tuna almasi, ambavyo ni precious stone, pia tuna Semi-precious Stone, tuna Ruby, Emerald, Green Garnet, Aquamarine, Honey Color Opal, Black Opal, Rhodolite, Moon Stone, tuna madini ambayo unaweza kuyataja mpaka ukaimaliza dunia yote yako ndani ya nchi yetu ya Tanzania, lakini hatuendi kwa speed inayotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimegundua jambo moja. Jambo la kwanza, natural resources haiwezi kufanya kazi yenyewe bila human resource. Unapokuwa na madini, lazima uwe na akili ya kuyageuza madini hayo kuwa barabara, maji au umeme. Kwa hiyo, naweza kusema basi, human resource is superior to natural resources, kwa sababu unahitaji binadamu ili ageuze hizi natural resources kwenye maisha kamili ya watu ya kila siku. Nikaona hili ni tatizo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la pili ambalo nataka kuliongelea kwa dakika zangu hizi chache, Tanzania tunashindwa kuendelea mbele kwa kasi kwa sababu hatuna mwendelezo wa regime moja kutoka regime nyingine. Ni kana kwamba Mheshimiwa Nape Mbunge wa Mtama alikuwa amedukua hotuba yangu; sijui kama ni mtalaam wa IT au hapana, kwa namna nyingine nafikiri ama aliona maono ama alifanya udukuzi fulani ambao nitaufuatilia baadaye. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilichotaka kusema ni hiki, hebu tuone; Rais wa Kwanza wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mwl. Julius Kambarage Nyerere, alitawala kwa miaka 24. Wakati anamaliza utawala wake, aliacha viwanda 411 vinafanya kazi. Unaweza kuvitaja, Kiltex, Musomatex Mwatex Sunguratex, you can name vyote, viwanda vilikuwa vinafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, amekuja Mheshimiwa Rais wetu wa awamu ya pili kama alivyosema Mheshimiwa Nape ali-improve baadhi ya mambo, lakini hakuendelea na wazo la viwanda, palikuwa kimya. Akaingia Rais wa tatu, viwanda vilevile vilivyoachwa na Mwalimu badala ya kuviendeleza, akaanza kuvibinafsisha vikauzwa vyote vikaondoka. Kwa hiyo, hakuna muunganiko kati ya regime ya kwanza na regime ya tatu. Tutakesha kama hakuna muunganiko huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, haikutosha, amekuja Rais nne ambaye ni Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kiwete ambaye hatukumwona akishughulika na viwanda hata kidogo, tulimwona akishughulika na mambo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukamwona Rais anayefuata, Mheshimiwa John Pombe Magufuli, tena anasema, “Tanzania ya Viwanda.” Viwanda vilevile ambavyo Mzee Mkapa alivibinafisha na kuviuza, huyu tena anasema Tanzania ya Viwanda. Hapo ndipo tunaanza kupambana tena kuanza viwanda wakati viwanda vimebinafsisha, vimeingia mikononi mwa watu binafsi, nao awajajenga viwanda bado.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nikagundua jambo moja ambalo napenda niliseme. Kila Rais aliyeingia madarakani ali-perform vizuri colorful kwa namna yake; Mwalimu Nyerere ali-perform vizuri sana kwa namna yake; Mwinyi ali-perform vizuri sana kwa namna yake; Mkapa ali- perform vizuri sana kwa namna yake; Mheshimiwa Jakaya Kikwete ali-perform vizuri sana kwa namna yake; Mheshimiwa Magufuli aka-perform vizuri sana kwa namna yake; naamini na Mheshimiwa Samia ata-perform vizuri sana kwa namna yake pia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, namna zao hizi, kama kila mtu ana namna yake, unategemea nchi itaendeleaje? Kwa sababu kila mtu ana namna yake; na namna ya mmoja ni kinyume cha namna ya aliyetoka. Tutaendaje kama namna hizi hazifanani? Hii inanipelekea kusema, ili tuendelee, tunahitaji agenda ya pamoja ya Taifa lote. Kwa namna gani tu-define maono ya Tanzania ya miaka 30 ijayo. Inaweza ikawa miaka 30 au miaka 50, tuwe na vitu ambavyo sisi Watanzania tutaviita maendeleo. Siyo lazima vitu hivyo viitwe maendeleo Marekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ujenzi wa maghorof siyo maendeleo kwetu. Tunaweza kusema maendeleo kwetu ni kila Mtanzania awe na maji safi na salama. Tunaweza kusema maendeleo kwetu; kila Mtanzania mwenye uwezo wa kusoma shule, asome Chuo Kikuu na amalize, asiwepo asiyesoma Chuo Kikuu. Tunaweza kusema maendeleo kwetu sisi, wafanyabiashara wafanye biashara vizuri, tuwe na export. Tunaweza kutafsiri maendeleo tunayoyaita maendeleo katika nchi ya Tanzania na tukaacha kutafsiri maendeleo kutumia jukwaa la Wamarekani au watu wa Ulaya, tukaamua kuwa na miaka 50 ya kile ambacho sisi tunaamua kuki-achieve kama maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kila Rais anayeingia madarakani, aingie kutimiza kwa namna yake na kwa sarakasi yake vile vitu ambavyo sisi tumevitafsiri kama maendeleo kututimizia kwa namna yake. Kama hatutafanya hivi, tuna hatari. Kwa sababu Katiba yetu inampa nafasi kila Rais anayeingia madarakani kwa namna yake, kwa hekima yake na kwa namna anavyotafasiri yeye maendeleo awaletee maendeleo Watanzania. Siku moja tutakapopata Rais ambaye hayuko sawasawa, tutaishia kulia. (Makofi)

Mheshimiswa Naibu Spika, ni ombi langu sasa kwa dakika chache hizi, naomba ikiwa ni nia yetu tuendelee, tuwe na vision ya miaka 50 ya Taifa na hii vision tuitafsiri, tuseme vision yetu ni kila mmoja apate maji, kila nyumba iwe na umeme, asipatikane Mtanzania anayekaa kwenye nyumba ya majani; tu-define vision yetu. Halafu tunasema, inapoingia regime, anapoingia Rais, lazima ilani ya chama chake izungumze mambo ambayo sisi tumejiwekea kama maono ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano. Patakapotokea Rais akaanza kufanya mambo yake ambayo hayako ndani ya ilani, kuna mtu wa kumwuliza hapa Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi na Amirijeshi Mkuu kwamba hutakiwi kufanya hayo? Hayupo! Tutakapokuwa na vision ambayo imewekwa kwamba tunahitaji ku-achieve mambo kadha wa kadha na kila regime inapoingia, iwe ya kijani, ya blue au ya namna yoyote, itatimiza yale ambayo tumejiwekea kama maendeleo kwetu na maono ya Taifa letu. Tafuta sarakasi zako ama kwa ukali, ama kwa nguvu, ama kwa namna yoyote, ilimradi yale maono tuliyojiwekea kama Taifa yatokee kwa haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Ahsante sana. Nasema tena, katika jina la Mwenyezi Mungu Subhan- huwa-taallah na katika jina la Yesu Kristo na katika jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kazi iendelee.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia. Namshukuru pia Waziri wa Afya, Mheshimiwa Dkt. Dorothy pamoja na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dakika chache sana nizitumie dakika zangu vizuri. Nataka kuzungumza kwa habari ya chanjo zinazoitwa corona vaccine.

Mheshimiwa Nainu Spika, niseme kwa ufupi kwamba mimi siko kinyume na chanjo za corona, hapana, wala siko kinyume na chanjo yoyote ile. Kwenye mazungumzo yangu, mtu asininukuu kwamba napinga chajo, hapana, kwa sababu tayari Tanzania tulishachanjwa; chanjo ya Kifua Kikuu tayari tulishachanjwa; chanjo ya Surua tayari; chanjo ya Kifaduro tayari; chanjo ya Polio tayari; na sasa hivi kuna chanjo zinaendelea kama chanjo ya Homa ya Ini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, siko kinyume na chanjo kwa sababu tayari chanjo ziko Tanzania na watu wanaendelea kuchanjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu ambacho niko makini nacho sana ni aina ya chanjo inayoitwa chanjo ya corona virus ilivyokuja na study yake. Chanjo hii ni tofauti na chanjo nyingine zote ambazo zimekuwepo duniani. Dunia imekuwa na aina ya chanjo zinaitwa attenuation. Maana yake ni kwamba virus wa corona wanapunguzwa nguvu, wanaondolewa properties, halafu wanaingizwa ndani ya mwili wa mtu, halafu antibodies zina-react, immunity inatengenezwa. Hii ndiyo aina ya chanjo ambayo imekuwepo miaka yote na siku zote. Chanjo hii kukamilika inagharimu miaka minane mpaka kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, chanjo hii inayoitwa chanjo ya corona ni chanjo ya mwendokasi, miezi miwili, miezi mitatu au miezi minne tayari. Unapojaribu kuuliza kwamba hii chanjo kwa nini imekuwa na haraka sana? Kuna magonjwa mengi kama Malaria na mengine ambayo tungetegemea mfanye haraka haraka kupata chanjo ili watu waokolowe. Wanasema sababu ya kwanza, kwa sababu teknolojia imeongezeka; sababu ya pili, wame-mobilize resources kutoka kwenye makampuni mengi duniani; na sababu nyingine ni kwamba ni kwa sababu ni pandemic, nami sikatai.

Mheshimiwa Naibu Spika, tekhnolojia ya chanjo hii inaitwa MRA. Maana yake, ni aina ya chanjo ambayo wanachukua generic material ya virus halafu wanaingiza kwenye MRA ya mtu, baadaye mtu, wanasema kwamba hataingilia na gene, lakini wanasema wanaingiza kwenye genetical material yaani genetical material za virus zinaingizwa kwenye cell ya mtu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti ya mtu na mnyama ni RMA, DNA na GINOS ambazo ndio genes. Huo ni utu wa mtu tofauti na mnyama. Chanjo hii inaingia mpaka kwenye RNA, chanjo hii inaingia kwenye DNA, kwenye GINOS, kwenye utu wa mtu. Hatujajua baada ya chanjo hii atazaliwa mtu wa namna gani baada ya miaka kumi, baada ya miaka mitano, baada ya miaka sita, hatujajua mpaka leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati mbaya sana, nifunguke kidogo na hekima yako ikikuruhusu utaniongezea muda kidogo kama ukiisha, kwa sababu hoja yangu ina national concern. Mashirika duniani kwa mfano, Marekani kuna shirika ambalo linaruhusu dawa zianze kupitishwa, linaitwa CDC (Center for Disease, Control and Prevention).

Mheshimiwa Naibu Spika, shirika lingine linaitwa FDA ambayo ni Food and Drug Administration; haya ndiyo mashirika ya Kimarekani yanayo-authorize dawa zote kwa ajili ya matumizi ya binadamu. Chanjo hizi zote unazoziona, hazijawa authorized na mashirika haya. Kuna kishirika kidogo ambacho kinaitwa Emergence Use Authorization.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiki kishirika kinaidhinisha dawa ambazo ni dharura, ambazo zinatakiwa ziende haraka. Sheria ya hawa Emergences Use Authorization ni kwamba kwa sababu dawa haijafanyiwa utafiti wa kutosha miaka mingi, kwa hiyo, inaruhusiwa emergence kwa sababu ya uhitaji wa dunia. Madhara yatakayowapata wale, liability haziko juu ya hii kampuni, ziko juu ya mtumiaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa najaribu kuwaza, nikiangalia kwa mfano chanjo ambazo ziko tayari zimesharuhusiwa kuanza kwa mfano, kuna chanjo ya kwanza inaitwa Jonhson Johnson, imeruhusiwa na Wamarekani ambayo tarehe 27 Februari, 2021 ndiyo ilikuwa authorized kutumika emergency, lakini kwenye website yao, watengeneza chanyo wenyewe wanasema madhara au side effect ya chanjo hii: kwanza, kushindwa kupumua sawasawa; pili, kuvimba kwenye uso na kwenye throat; tatu, mapigo ya moyo yanakwenda haraka; nne, bad rush kwenye mwili; tano dizziness; na sita, damu kuganda kwenye mwili. Hii ni kwenye website yao. Sasa kama watengenezaji wa chanjo wenyewe wanaonesha kwenye website yao kuna shida hiyo, ni vizuri sasa tuwe makini. Najua Mheshimiwa Rais kwa hekima yake ameunda Kamati inayofuatilia hayo, lakini mimi kama Mbunge nina haja ya ku-discuss na ku-alert kwamba wawe makini wanapochagua aina ya chanjo hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nyingine ya pili inaitwa AstraZeneca, ambayo imetengenezwa Oxford kule UK. Yenyewe kwenye website yao wanasema side effect yake ya kwanza ni damu kuganda; na ya pili ni kifo. Ni kifo ndiyo. Wanasema, kwenye kifo hapa, wanaweza kufa watu labda kumi out of hundred, lakini kwenye website yao wanaonyesha kwamba death may occur, lakini dunia bila kufanya research, bila kuwaza watu wanakimbilia kupata chanjo kwa sababu ya fear ya corona.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyingine inaitwa Moderna ambayo ni ya USA na nyingine inatiwa Pfizer ambayo ni ya Ujerumani. Kwa ujumla chanjo hizi zote zinaonyesha side effect ni kuganda damu, kushindwa kupumua na kifo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni kweli, tukikataa chanjo tunaweza kuwekewa ban ya kusafiri kwenda Ulaya kwa sababu hatujachanjwa. Tunakabiliwa na uchaguzi mbaya sana; tuchanjwe kitu tusichokijua sawa sawa au tusichanjwe tuzuiwe kwenda Ulaya. Naomba sana Wizara ya Afya wajaribu kuangalia kwa makini sana kwenye suala ya chanjo. Waangalie madhara ya sasa, madhara ya siku zijazo na madhara ya Taifa. Jambo hili ni la muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niruhusu kidogo niongeze kidogo. Matatizo tuliyonayo ni kufikiri kila kinachotoka Ulaya kinafaa kwetu; and this is a problem we face. Our colonizers (watawala wetu) walitujengea ufahamu kwamba kikitoka kwao kinafaa. Jana kuna mtu mmoja anaitwa Dkt. Edward Fleming ambaye ni kati ya watu walioshiriki kutengeneza mojawapo ya chanjo, alikuwa ameandika barua kwa Rais wa Marekani, nina rekodi, amesema, anashauri hizi chanjo ziachwe mara moja kwa sababu madhara yake ni makubwa kuliko faifa yake kwa prevention. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naiomba Serikali yangu sikivu pamoja na Wizara ya Afya, before we venture in to what kind of vaccine we should take, tunatakiwa tuwe na wataalam wetu wa hapa. Namba moja, wa-analyse content. Haya majina ya chanjo ni business name, lakini kuna generic name that includes the content, kuna nini ndani ya chanjo, wa-analyse matatizo yatakayotupata sisi tutakaochanjwa na watoto wetu baadaye. Kwa sababu shida ikiingia kwenye DNA na kwenye gene na RNA, ndiyo utu wa mtu. Ina-send message miaka ijayo mtu azaliwe wa namna gani? Madhara yanaweza kuwa siyo leo, but in 20 or 30 years to come tunaweza kuwa na Watanzania wasioweza kufikiri vizuri, wasio na maamuzi mazuri na Taifa letu litashindwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sana Wizara ya Afya, before we know which method we implement, tufanye due-diligence ya kuifuatilia hii chanjo ni ya namna gani? Pia tusome website.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niongezee jambo moja kwamba anything kule Marekani au kule Ulaya; Ulaya kuna organization inaitwa EMA maana yake ni European Medicine Agents ambayo na yenyewe ina- authorize dawa zote ndiyo zinatumika. Hizi agency zote; agency ya Ulaya na agency za Marekani hazija-authorize zenyewe, zimewekwa kwenye ka-institution kanakoruhusiwa kuwa-authorize emergence kule na matokeo ya kuwa-authorize emergence, huyo aliyetengeneza dawa hana madhara, kwamba ni wewe mwenyewe, utajijua wewe mwenyewe; na wanasema kwamba iwe inatumika huku inafanyiwa uchunguzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ujinga kuruhusu Taifa zima kuwa experiment ya majaribio, eti kwa sababu tuna haraka ya Corona. I know Corona is dangerous, yes but it is more dangerous for us to allow the all natives, Watanzania wote milioni 50 wachanjwe eti ndiyo tuwe tunaangalia matokea, tunaripoti kwenye hizi institution. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sana hili suala liangaliwe kwa makini, lifanyiwe kazi na mwisho wa siku kila silaha itakayofanyika juu yetu haitafanikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie kwenye hii hoja ya Kamati ya Viwanda, Biashara, Uwekezaji pamoja na Mazingira. Kwa maksudi ya kuokoa muda nitachangia kwenye suala la Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba nizungumze kwa malengo ya kusaidia nchi na ninaomba nieleweke vilevile kwamba mchango wangu unalenga kuisaidia nchi tuipendayo ya Tanzania na kumsaidia Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan. Hivyo ndivyo ninatakiwa nieleweke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili la mradi wa Liganga na Mchuchuma ulianza mapema sana mwaka 2007 tena kwa Waraka Na. 14/2007 wa Baraza la Mawaziri. Katika kutafuta watu watakaofanya hii kazi Kampuni 48 zilijitokeza. Wakati naendelea nina-declare interest kwamba mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji, kwa hiyo naongea mambo ambayo nayafahamu vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni 48 zilijitokeza kwa ajili ya kuomba kufanya hii kazi, ni kampuni moja tu peke yake ambayo ilikuwa tayari kuchukua project ya Liganga na Mchuchuma, kampuni zingine zote 47 zilitaka zifanye makaa ya mawe peke yake. Hii kampuni peke yake ambayo ilijitokeza yenyewe ifanye miradi yote miwili Liganga na Mchuchuma ambayo ilikuwa ni Sichuan Hongda ya China.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kampuni baada ya kutokea, kampuni hii ikaanza kazi na tayari Serikali ikaamua kupitia Wizara ya Viwanda na Biashara itengeneze timu maalum yenye uwezo wa kusimamia hili jambo. Timu iliyotengenezwa High Technical Committee ilikuwa ina-include watu wafuatao: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaisoma hii High Technical Committee kukuonesha kwamba waliokuwa wanashughulika na jambo hili siyo mazuzu, ni watu wenye uelewa, ni watu wenye elimu, ni watu wenye heshima katika Taifa letu la Tanzania. Ilitengenezwa committee hii ambayo wa kwanza alikuwa ni Kamishna wa Madini kutoka Wizara ya Madini ndiye alikuwa Mwenyekiti; pili, alikuwa Kamishna wa Nishati kutoka Wizara ya Nishati na Madini; Tatu, alikuwa Mkurugenzi wa Viwanda kutoka Wizara ya Viwanda, mwingine alikuwa Mkurugenzi wa Uendeshaji wa Shirika la Taifa la Maendeleo (NDC), mwingine alikuwa Kamishna wa Sera kutoka Wizara ya Fedha, mwingine alikuwa Mchumi Mwandamizi kutoka Wizara ya Maendeleo na Miundombinu, Mwingine alikuwa Mkurugenzi Msaidizi wa Mipango na Ukuaji kutoka Wizara ya Mipango na Uwezeshaji, mwingine alikuwa Afisa Mipango Mwandamizi kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, mwingine alikuwa Mkurugenzi wa Mikataba ya Kimataifa kutoka Ofisi ya Mwanasheria wa Serikali, mwingine alikuwa Mkurugenzi wa Export Processing Zone Authority na mwingine alikuwa ni Mkurugenzi Mtendaji wa Tanzania Investment Center na mwingine alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa STAMICO na mwingine alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa RAHCO, Mwingine alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa ndiyo waliochaguliwa kuwa technical team ya kuongoza hili suala la Liganga na Mchuchuma, hawa siyo watu wadogo. Nataka kuondoa notion kwamba eti Serikali iliingia kwenye mikataba bila kujua no! Hawa watu ni wataalam, waliochaguliwa kwenye technical team ili kwamba waongoze suala la Liganga na Mchuchuma kufikia mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maksudi ya kuisaidia nchi yetu na vizazi vijavyo wakakubaliana huyu Sichuan Hongda - Mchina kwa ubia na Shirika la NDC la Serikali walikubaliana mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, walikubaliana kwenye mkataba wao wa awali kwamba Serikali ya Tanzania kupitia NDC ichukue asilimia 20 na huyu bwana achukue asilimia 80. Sasa baadae kukawa na ubishani kidogo kwenye hiyo percent, kwamba hapana ni kidogo sana baadae wakakubaliana kwamba iwekwe annex kwenye huo mkataba kwamba Tanzania baadae ina uwezo wa kununua share ikafikia asilimia 50, ili kwamba sisi kama Taifa tuwe na hamsini na huyu mwekezaji awe na hamsini, that was very good.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikufungue macho, mradi huu una jumla ya thamani ya dola bilioni tatu. Kama nchi ya Tanzania ingeweza kuchukua share ya asilimia 20 maana yake tungepata dola milioni 600 kila mwaka. Lakini mradi huu unadumu kwa muda gani, mradi huu kwa mujibu wa deposit unadumu kwa muda wa miaka 100. Kwa hiyo, Taifa la Tanzania lingepata dola milioni 600 mara miaka 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tulikuwa tumefanikia ku- score kwamba tutanunua share zingine ili Taifa letu liwe linapata asilimia 50. Kama Taifa letu lingekuwa linapata asilimia 50, kila mwaka tungekuwa na uwezo wa kupata dollar 1.5 billion kila mwaka mara miaka 100! Narudia tena mara miaka 100 - this is documented. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni makosa ya hali ya juu sana kuona bado mradi huu haujaanza mpaka leo, wenye uwezo wa kuipa Serikali fedha nyingi kiasi hiki kwa mambo ambyo nitayeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kilichotokea ni kwamba huyu mwekezaji alikuwa tayari na Serikali kupitia NDC tukasaini performance contract, tukakubaliana naye tayari kwa ajili ya kuanza. Baada ya kusaini performance contract, mwekezaji akawa na wasiwasi baadae akasema bwana mimi naomba mnipe incentive zaidi kwa sababu ya uwekezaji wangu mnipe incentive zaidi ili kusudi niweze kupeleka huu mradi.

Kwa hiyo, Serikali ikasaini tena performance contact ya pili na huyu mwekezaji kukubaliana na hizo incentives ambazo huyu mwekezaji alikuwa ameomba. Performance contact ya pili ilisainiwa 30 Juni, 2014 tukasaini sisi wenyewe kwamba tumekubaliana naye ili apate incentives zingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hapo inabidi sasa hizi incentive alizoomba mara ya pili ziwe gazetted. Haziwezi kufanya kazi bila ya kuwa gazetted na Wizara ya Fedha. Hazijawa gazetted mpaka leo kwa nini? Hazijawa gazetted mpka leo, matokeo yake tunaanza kusema kwamba huyu mwekezaji ni tapeli, huyu mwekezaji hajulikani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza kukupa ushahidi, Kamati hii ilisafiri kwenda mpaka China ikamtembelea huyu mwekjezaji, ikafika kwenye ofisi zake, ikafanya due diligences, ikapaona alipo. Inawezekanaje tunaweza kusema leo tuache mradi huu wenye uwezo wa kutupatia 1.2 billion dollars mara miaka 100.

MHE. CHRISTOPHER OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKLITI: Mheshimiwa Ole-Sendeka, taarifa.

T A A R I F A

MHE. CHRISTOPHER OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimu sana Baba Askofu. Ninaufahamu mradi huu wa Liganga na Mchuchuma kama ninavyo kifahamu kiganja cha mkono wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna mradi ambao Serikali ikitekeleza ni mradi wa kifisadi ni mradi huu wa Liganga na Mchuchuma kwa hali mkataba ulivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo ni wa dola bilioni tatu na ilitakiwa ikopwe dola bilioni 2.4 kwa kugawana kati ya Kampuni ya Tanzania na Kampuni ya China halafu Wachina waje na bilioni 600 tu. Kwa kuleta kwao bilioni 600 iwastahili wao kupata asilimia 80 ya mapato wakati deposit ni yetu lakini ile bilioni 2.4 tunalipa sawa kwa sawa. Kama tunalipa sawa kwa sawa kwa nini mapato hatugawani sawa? Kwa nini mimi Tanzania nipewe 20 kwa chuma changu chote cha Liganga halafu kampuni ya Wachina ichukue asilimia 80? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nikwambie huu ni mpango wa kifisadi mchana kweupe. Nataka nikwambie kama kuna kampuni ilikuwa inapiga deal ya kuiumiza nchi hii ni kampuni hiyo ya Chuan Hong Da. Nataka nikwambie hoja ziililetwa hapa Bungeni na waliokwenda China watuambie nani aliwapeleka na ripoti ya China ije hapa. Hawa ni mafisadi mchana, mimi nitaweka mezani ushahidi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Josephat Gwajima unaipokea hiyo taarifa?

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru sana kaka yangu nimwambie waziwazi anaongea bila kujua anachoongea. Mimi hapa nina document ninaweza ku- supply document kwenye Bunge lako moja baada ya nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nisikilize kwanza sisi wenyewe kama Serikali tumesaini arbitration document…

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nyongo taarifa.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimtaarifu kaka yangu Mchungaji kwamba mradi huu bahati nzuri mimi nimekwisha kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Viwanda na Biashara na kwa bahati nimekwisha kuwa Naibu Waziri wa Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, deposit iliyopo Liganga na Mchuchuma makaa ya mawe kuna tani zaidi ya milioni 400 na mradi mzima kwa maana ya chuma pamoja na makaa una cost dola za Kimarekani bilioni tatu. Mwekezaji amekuja na milioni 600 tu; bilioni 2.4 tumpe guarantee ya Serikali tukope naye, hilo moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na incentives alizokuwa anaziomba ambazo Mheshimiwa Mchungaji anazisema, mradi ule ulikuwa uzalishe megawati 300 za umeme, megawati 250 alitaka Kumuuzia TANESCO na katika kumuuzia TANESCO alitaka aweke mtambo wa kuzalisha umeme na mtambo ule alitaka tumlipe capacity charge, at the same time amuuzie TANESCO umeme kwa senti dola 11. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huo tungesema tuukubali ulikuwa unakwenda kutafuna nchi yetu kwa sababu deposit ni yetu, chuma ni yetu, tulikuwa na uwezo wa kumpa hata STAMICO akachimba akaweza kuuza ule mkaa na akazalisjha umeme na aka-supply kwenye chuma ambapo ni kilometa 80 kutoka kwenye makaa ya mawe kwenda kwenye chuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali iutazame tena mradi huu upya, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Josephat Gwajima unaipokea hiyo taarifa?

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa yake, labda nimpe shule zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu ulikuwa ndani yake na miradi kama mitano; mradi wa kwanza ni kuchimba chuma na kutengeneza chuma; mradi wa pili, kuchimba makaa ya mawe; mradi wa tatu, kutengeneza umeme megawati 600; megawati 300 na megawati 300 ziingie katika Gridi ya Taifa; mradi unaofuata wa nne, kutengeneza barabara ya lami kutoka Mchuchuma kwenda Liganga. Hiyo ndiyo miradi iliyokuwepo pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikiliza ninaomba kama anafikiri mimi ninabahatisha mikataba iletwe hapa Bungeni uone maajabu yaliyopo. Kwanza tayari tuko kwenye matatizo na kama angeweza kunisikiliza ushauri wangu mpaka mwisho ingeokoa taifa hili kupelekwa arbitration. Tutapigwa halafu tutaumia wakati kuna njia ya kutokea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba ufanye hivi, huyu mtu ambaye sisi tulimuona ni tapeli, ilikuwaje tukasaini mikataba hii? Ilikuwaje tukaenda mpaka China kutembelea kampuni yake na tuka-approve? Imekuwaje viongozi hawa niliowataja wote wakuu wa mashirika ya umma wakasaini na mpaka leo mkataba uko valid, ilikuwaje? What happened?

WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Gwajima kuna taarifa ya Mheshimiwa Waziri wa Viwanda na Biashara.

T A A R I F A

WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango mzuri anaoutoa Mheshimiwa Gwajima, lakini nikitambua taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Ole-Sendeka, taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Nyongo, naomba kumpa mzungumzaji taarifa nikitambua yeye ni Mjumbe wa Kamati yetu ya Viwanda, Biashara na Mazingira kwamba tuliyoyawasilisha kwenye Kamati ndiyo maelezo mahususi ya Serikali na kupitia mchanganyiko huu unaoonekana mbele ya Bunge lako ndio Serikali yetu kupitia viongozi wetu wakuu wote, Rais wa Awamu ya Nne, Rais wa Awamu ya Tano, Rais wa Awamu ya Sita wakiwa na lengo la kutekeleza mradi huu, lakini kwa maslahi mapana ya Taifa ndipo walipoelekeza mikataba hii iweze kufuatiliwa kwa sababu kama anavyosema Mheshimiwa Gwajima addendum iliyosainiwa, GN haiwezi kutolewa kwa sababu iko kinyume na sheria za nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa yangu naomba pia aweze kuipata Mheshimiwa Gwajima ndio maana wale uliowasoma waliokuwa kwenye timu mpaka sasa wako kwenye vyombo vya uchunguzi wanafanya kazi kujiridhisha ni nini kilichotokea mpaka kufikia hapo walipofikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa hii Mheshimiwa Gwajima. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Gwajima kwa dakika moja naomba uhitimishe hoja yako kama unapokea taarifa au hupokei.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikubali kwamba maelezo aliyotoa Mheshimiwa Waziri, ni wajibu wake wa Kiserikali kufanya hivyo, lakini mimi msimamo wangu uko pale pale na natoa angalizo namna utakavyofanya kwenye namna ya kusitisha mkataba na huyu mwekezaji, iangaliwe kwa umakini sana kwamba Serikali isije ikaumizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi kwa makusudi ya kulifanya Bunge lako na kamati yetu iwe sawa sawa niko tayari kuwasilisha document zinazoonesha kwamba hapa tulipo si pazuri sana. Nakushuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana kwa kunipa hizi dakika chache za kuchangia katika hoja ya Wizara ya Uwekezaji, Viwanda pamoja na Biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anafanya kazi kwa bidii kuwapigania Watanzania na kulipigania Taifa letu, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwashukuru ndugu zangu Mawaziri kwa namna wanavyofanya kazi kwa bidii kumsaidia Mheshimiwa Rais ili kutimiza ndogo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuchangia kwenye hoja iliyo mbele yetu ya Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Nataka nijikite sana kwenye suala la Liganga na Mchuchuma. Liganga na Mchuchuma imekuwa hoja ya muda mrefu sana pengine watu hawajui Liganga ni nini? Unaposema Liganga ni mlima wa chuma, ni mlima wa iron ore, si chuma ya kuingia chini kuchimba ni mlima wa chuma na uposema Mchuchuma ni mlima mwingine wa makaa ya mawe ambavyo hivi viwili mlima wa chuma pamoja na mlima wa makaa ya mawe ya kuiyeyushia hiyo chuma yamewekwa na Mwenyezi Mungu kwenye eneo moja ili kazi iwe rahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana, ni vizuri pia kugundua kwamba, uzinduzi wa Liganga umefanyika 1860 karne ya 18, hiki chuma cha Liganga kikagunduliwa hapa Tanzania na uvumbuzi wa hii Mchuchuma kwa maana ya makaa ya mawe ni 1898. Ina maana Mwalimu Nyerere akiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alikuwa anajua, Mzee Mwinyi alikuwa anajua, Mzee Mkapa alikuwa anajua, Mzee Jakaya Kikwete alikuwa anajua, Mzee Magufuli alikuwa anajua na Mama yetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan pia anajua kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kujiuliza ni kwa nini pamoja na hiki chuma kugunduliwa muda mrefu karne ya 18, lakini hatujachimba na mahitaji ya chuma ni makubwa hapa Tanzania, ni kwa nini hasa? Kwenye kuzungumza kwangu kwa dakika chache nitawagusa baadhi ya watu siyo kwa ubaya bali kwa lengo la kusaidia nchi yetu. Nipo hapa Bungeni kwa lengo la kusaidia nchi na si vinginevyo. Kwa hiyo katika kuzungumza nikimgusa mtu nisifahamike nimemgusa kwa ubaya bali nimemgusa kwa maslahi mapana ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nitoe takwimu kidogo ya uingizaji wa chuma Tanzania. Kwa mfano, mwaka 2018 tumeingiza chuma cha thamani ya dola milioni 401.2 hapa Tanzania, tumenunua sisi. Mwaka 2019 tumeingiza chuma ya thamani ya dola milioni 491.9 hapa Tanzania. Mwaka 2020 tumeingiza vyuma vya thamani ya dola ya milioni 423.4 hapa kwetu Tanzania. Mwaka 2021tumeingiza chuma ya dola ya thamani ya milioni 7.8. Mwaka 2022 tumeingiza chuma ya thamani ya dola milioni 235.7 hapa kwetu. Kwa hiyo kwa miaka hii mitano tumelipa fedha ya kigeni kutoka Tanzania kwenda nje ya nchi kwa ajili ya chuma, dola bilioni 2.2 kutokea hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtu yeyote mwenye akili na anayejua kuzitumia, jambo hili haliwezi kuruhusu kufanyika kama chuma ipo hapa Tanzania. Sasa unihurusu niongee machache kidogo, ni kwa nini sasa hili jambo halijafanyika? Hebu nikupe mawazo, kwamba, tumeanza na reli, ujenzi wa reli standard gauge a good idea very good idea na si kinyume na hapo. Kwenye ujenzi wa reli, component kubwa inayotumika ni chuma, sasa ilikuwaje tukaanza kujenga reli kwa kuagiza chuma kutoka nje ya nchi badala ya kutengeneza chuma chetu kwa kuchimba ndiyo tukaanza na reli, ilikuwaje? Ni kitu gani kinatokea mpaka priority ya kwanza inakuwa ya mwisho na ya mwisho inakuwa ya kwanza. Kinachosumbua ni kukosa Maono ya Taifa, Mipango ya Taifa na Dira ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, simlaumu mtu yoyote. Nataka sasa unisikilize vizuri, kwa mfano, kama kungekuwa na maono ya Taifa juu ya viwanda maana yake kungekuwepo maono ya muda mrefu yanayoelezea juu ya chuma kilichopo Tanzania. Kwa hiyo, tusingekuwa tumeanza na reli, tungekuwa tulianza na fedha ya kuchimba chuma ili chuma chetu kije kitengeneze reli zetu, tungeokoa mabilioni ya shilingi tunayoyasema hapa. Nchi yetu inahitaji maono au agenda ya Taifa ya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sikiliza, jambo hili linaonekana kwamba its nonsense, its chasing wind lakini sikiliza niwaambie nchi nyingi zilizoendelea zina maono ya nchi zao ya muda mrefu. Hakuna nchi duniani iliyoendelea kwa muda wa miaka mitano au kwa muda wa miaka kumi. Nchi huwa zinaendelea kwa kuweka maono ya miaka mingi, unaiona nchi kwa mbali, wanafunzi wataiona nchi kwa mbali, wasomi wataiona nchi yao kwa mbali. Tukifanikiwa kuiona nchi kwa mbali tunaweza kuisukuma Tanzania kuipelekea mahala ambapo inatakiwa kuwa.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa, Mheshimiwa Kingu.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa msemaji kaka yangu Askofu Gwajima, kuonesha kwamba pia kuna mahali tuliteleza, sisi tumefuta hata tume hiyo ya kutengeneza mipango ya muda mrefu wa nchi. Leo tunapozungumza kwenye Taifa letu hatuna kitu kinaitwa Tume ya Mipango ambayo ndiyo wanatengeneza plans za nchi za miaka hamsini na kwenda mbele, we don’t have Tume ya Mipango.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Gwajima, taarifa hiyo.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mheshimiwa Kingu ana taarifa nyingine za namna hiyo aendelee kunipa, naendelea kuzikubali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kinachosumbua sana ni mipango ya muda mrefu. Tungekuwa na mpango wa muda mrefu wa hii Mchuchuma ni aibu. Nikupe mfano; kuna Paris Agreement on the use of coal ambayo imeweka ukomo wa kutumia makaa ya mawe na ukomo huo ni 2030. Hebu jaribu kuwaza tangu makaa ya mawe ya kwetu yamevumbuliwa karne ya 18 mpaka yanataka kufikia ukomo hatujayatumia bado, what can you call this, hiki kitu unaweza kukiitaje? Kwamba Mungu amewawekea mlima wa chuma, halafu amewawekea moto wa kuyeyusha hiyo chuma palepale, hamwezi kuitumia mpaka unafika wakati umefika ukomo wa kutumia 2030, hatujaitumia, jambo hili hatutakiwi kuliruhusu hata kwa dakika moja, hata kwa sekunde moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini kinatuleta mpaka hapa, kukosa maono. Naomba viongozi wetu waliopo Mawaziri, Naibu Mawaziri waliopo Serikalini pamoja na mama yetu mwema, mama anayewapigania Watanzania, mama Samia Suluhu Hassan, zawadi peke yake tunayoweza kuipa nchi hii kwa sasa hivi ni maono ya nchi ili watu waweze kuiona nchi kwa mbali nawaweze kupanga mipango yao sawasawa na maono ya nchi…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Gwajima subiri kidogo, Mheshimiwa Waziri.

T A A R I F A

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitambue mchango mzuri anaoutoa Mheshimiwa Mbunge na Mtumishi wa Mungu Askofu Gwajima; lakini nilitaka niweke tu kumbukumbu sawa kwamba Taifa letu mara zote limekuwa na mipango ya muda mrefu na mara zote tangu uhuru limeongozwa na viongozi wenye maono. Kumbukumbu mbili hizo; moja, tumekuwa na mipango ya muda mrefu na ndiyo maana tulikuwa na Dira ya 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Dira ya 2025 ilitungwa wakati wa Mkapa na miaka yote hii ikamegwa kwa miaka mitano mitano; na utekelezaji wake ukianza na dira ya kwanza, na ya pili na hata tunayoenda kumalizia, ilikuwa na mtiririko ambayo ukienda kwenye headings zake zimeongelea mpaka na hizi habari za viwanda, habari hizi zote ambazo tunaongelea za kukuza uchumi na hata sasa tunapomaliza 2025 tayari tumeshaanza kuandika dira nyingine ambayo kimsingi kwenye mijadala tunaangalia ama tuandike kwa utaratibu wa miaka 20, 20 au tuandikie tuoanishe na Dira ya Afrika iende 2063. Kwa hiyo, mipango ya muda mrefu ipo kwenye nchi yetu na hii ndiyo inayozaa utekelezaji huu wote ambao tunaoufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa maono, nchi yetu isingeongozwa kwa maono tusingekuwa hivi tulivyo leo, imeongozwa kwa maono ndiyo maana tumefika hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambieni ndugu zangu Watanzania, tusipende kujidharau, nchi zote majirani; SADC na Afrika Mashariki wanapenda maono ya Tanzania. Actually, wao wanaiona Tanzania ndiyo mfano. Kwa hiyo, tusijidharau. Ila tunapopeana fursa za kujirekebisha zaidi, turekebishe ili twende kwa kasi zaidi, lakini siyo kwamba nchi haijawahi kuwa na viongozi wenye maono na kwamba nchi haijawahi kuwa na mipango. Nchi nyingi tu hata mipango wanayotekeleza mingine wame-copy kutoka Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niliona tu niyaseme hayo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri naamini umeeleweka. Mheshimiwa Askofu Gwajima, taarifa ya Mheshimiwa Waziri hiyo.

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikimalizia, kwa mfano sasa hivi, Mheshimiwa Rais tayari ameshaweka kwenye pipe line utekelezaji wa hii miradi mikubwa, yote hii tunaenda kuitekeleza. Tunatekeleza Liganga, tunatekeleza LNG; hivi tunavyoongea, inaenda kutekelezwa siku siyo nyingi. Yote hayo ni maono na ni utekelezaji wa mipango…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri, nafikiri umeeleweka, taarifa hiyo Mheshimiwa Gwajima.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimjibu kaka yangu Waziri wa Fedha na Mipango kwa staha kubwa kwa sababu yeye ni mwakilishi wa Serikali. Amethibitisha tu kwamba Mpango uliyopo ni mpaka 2025 na wanajiandaa kuandika Mpango mwingine. Amenithibitishia kwamba hatuna mpango wa miaka 50, hatuna mpango wa miaka 100. Kwa hiyo, namshukuru sana kwa kunisaidia kwa hilo. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikae kwenye hoja yangu. Ninachosema mimi, sidharau kilichofanyika na Serikali. Ninachosema, tukiwa na mipango ya miaka 50 au miaka 100, wanafunzi wakaiona nchi yetu kwa mbali; kwa mfano tukiwa na mipango ya muda mrefu...

MWENYEKITI: Mheshimiwa malizia, muda ulikuwa umeenda, lakini malizia dakika moja.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naona nikichangia muda unapungua, itabidi niombe Kanuni muda unapopungua inakuwaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema tu kwamba kwa ufupi tukiwa na mipango ya muda mrefu juu ya viwanda, wanafunzi wanaosoma shule wataiona nchi yao kwa mbali na watajua wasome nini kwa sababu wanaweza kuyasoma maono ya Taifa. Hicho ndicho ninachosema. I am not attacking anybody, I am trying to improve kwamba mahali tulipo ni pazuri, lakini tukiwa na mipango. Tungekuwa na mipango juu ya hili, tungekuwa tumeanza na kuchimba chuma chetu ili chuma chetu kitumike kwenye reli, hii fedha 2.2 billion dollars iliyoenda nje kununua chuma ingekuwa imebaki hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa muda na mimi nichangie hii hoja ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. mimi nitazungumza kwa uchache sana kwa habari ya Utawala Bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo ambalo linafanya tasnia nzima ya Utawala Bora katika nchi yetu iwe na dosari kubwa sana sana. Kuna hizi sheria, hii ya The Anti Money Laundering CAP 423 ya mwaka 2006 ambayo ilifanyiwa marekebisho na Bunge hili mwaka 2019, inajulikana kama Sheria ya Utakatishaji Fedha na hii Sheria ya Economic and Organization Crime Act. ambayo CAP 200 ya mwaka 1984 ambayo pia ilifanyiwa marekebisho na Bunge hili mwaka 2019 pamoja na Sheria ya Ugaidi ambazo zinafahamika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi sheria tatu zinaifanya dhana ya utawala bora katika nchi yetu itiliwe maswali sana. Kwa mfano Bunge hili wakati linapitisha sheria hii au kufanyia marekebisho sheria hii na sheria hii kufikia mahali kwamba haina dhamana kabisa, nia ya Bunge ilikuwa nzuri, lakini katika utekelezaji wake imeingia dosari nyingi sana, kuna watu wengi sana wapo ndani, wapo mahabusu maelfu ya watu kwa sababu ya hili suala la utakatishaji fedha, kubambikiziwa na watu wasio waaminifu katika vyombo vyetu vya dola na kwenye nchi yeyote makini jambo hili haliwezi kuachiwa hivi hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta mtu anakwenda kwa mfanyabiashara kukusanya mapato au kudai mapato au malimbikizo ya mapato anakwenda na charge kabisa anamwambia bwana usiponipa fedha kadhaa tayari nina hati hii hapa ninakuwekea money laundering au ninakuwekea economic sabotage kuna watu wengi sana wapo ndani, wapo mahabusu kwa sababu ya matumizi ya mabaya ya hawa watu wasio waaminifu ambao tumewakabidhi kuitekeleza hii sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka leo kwa mujibu wa takwimu kuna watu 1,701 ambao wako mahabusu kwa sababu ya ama kwa ajili ya money laundering au kwa sababu ya economic sabotage na kwa sababu hiyo nilikuwa nafikiri ni muhimu sana, kwakuwa kazi moja wapo ya Bunge letu ni kutunga sheria lakini na kufanyia marekebisho sheria na kufuta baadhi ya sheria, haileti sense kwa nini mpaka leo wale Masheikh 23 wa Uamsho wa Zanzibar wapo ndani mpaka leo mahabusu, leo ni miaka tisa, haileti sense kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najaribu kuwaza ningekuwa mimi au angekuwa baba yangu, au angekuwa ndugu yangu ambaye mpaka leo miaka tisa yupo ndani, hajahukumiwa bado na haijulikani ana hatia au hana hatia. Itakuwaje baada ya miaka 20 huyu mtu mkagundua hana hatia, atalipwa nini in-exchange na miaka aliyopoteza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi kwa kweli haliingii akilini kwanini hawa Masheikh 23 wa Uamsho wa Zanzibar wapo ndani mpaka leo kwa miaka tisa, lakini haitoshi kuna Masheikh 64 huko Arusha ambao nao wapo ndani kwa sababu ya hizi hizi Sheria za Ugaidi ambazo hazina dhamana kwa sababu ambazo hatuzielewi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nashangaa kwa nini Masheikh tu wapo ndani kwa ajili ya Sheria za Ugaidi hakuna gaidi mwingine ambaye sio Sheikh?(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Waziri husika pamoja na Serikali kwa ujumla tuangalie kwa undani sana namna ya kuli-handle suala hili, kwa sababu sio sahihi Masheikh hawa wakawa ndani kwa muda wa miaka tisa, sisemi kwamba wana hatia au hawana hatia sijadili kosa lao, lakini ninachojadili ni kwamba basi wangehukumiwa basi ikajulikana. Wangehukumiwa wangejua wamebakiza miaka mitatu/miaka minne/miaka mitano/miaka sita. Lakini sasa wapo ndani bila kujua watamaliza lini matatizo yao mimi nilikuwa naomba Wizara pamoja na by-imprecation Waziri wa hii Wizara ni Mheshimiwa Rais, na Mheshimiwa Rais wa nchi ni Rais wa nchi lakini pia ni Waziri wa hii Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba jambo hili lifanyiwe kazi, kuna watu wengi sana, rafiki yangu mmoja akanipigia simu akaniambia Askofu kuna watu wamekuja kwangu wananiambia ama niwape milioni 100 ama wanipe money laundering, nikamwambia wape haraka haraka utapata money laundering na utashindwa namna ya kutoka.

Nilikuwa nashauri sana sana kwa ajili ya kuondoa dorasi zinazotokana na kusemwa kwamba Tanzania hatuna utawala bora, tuweze kuziangalia kwa makini hizi sheria, tuzi- revise na naomba sana rafiki yangu Mheshimiwa Mchengerwa ulifanyie kazi hii Masheikh hawa 23 na Masheikh hawa 64 ambao wapo ndani utafute namna ya kufanya, vinginevyo nitakuondolea shilingi kwenye bajeti yako. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. ASKOFU JASEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia. Kwanza nikupongeze jana kwenye futari ya CRDB ulipendeza sana na nikaona umeanza kuitwa Ukti, keep it up utafika mahali pazuri sana. Lakini watu wengi sana waliochangia nataka nipate nafasi ya kuchangia hii hoja ya Wizara ya Elimu watu wengi sana waliochangia wamezungumza kwa habari ya curriculum au mitaala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mawazo ya watu wengi walikuwa wanachangia wakisema kwamba ni muhimu sana mitaala ya elimu hii kubadilishwa ili iwe skill basic curriculum na sikatai, lakini lipo jambo la muhimu sana ambalo ningependa ku-discuss it is a matter of national concern siyo jambo la tu Wizara ya Elimu peke yake lakini is a matter of national concern na hili jambo lina athiri Wizara ya Elimu directly as far less curriculum is concern.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba ninukuu mchangiaji wa jana aliyechangia anaitwa Mheshimiwa Nusrat Hanje alichangia jambo ambalo nanukuu alitoa kwenye Sera ya Elimu ya mwaka 2014 ambayo inasema kwamba lengo la elimu au objective ya elimu ni kumpa mtu maarifa, ustadi, umahiri, uwezo na mtazamo changa katika kuchangia maendeleo ya nchi. Hivyo ndivyo sera ya elimu ya mwaka 2014 inavyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaanza kuona kwamba objective ya elimu ni kumfanya mtu awe na maarifa awe na ustadi, awe mahiri, awe na uwezo na awe na mtazamo chanya katika kuchangia maendeleo ya nchi. Kwa hiyo, objective ya elimu ni maendeleo ya nchi sasa lipo jambo ambalo ni serious sana ambalo ningefikiri mtu yeyote msomi aliye kwenye Bunge hili anatakiwa aisaidie hii nchi na kizazi kijacho. Kama lengo la elimu ni kumsaidia anayepata elimu ni kuzalisha mtu ambaye ana uwezo wa kuchangia kwenye maendeleo ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, then maendeleo ya nchi ni nini, ni muhimu sana nchi hii iwe na maono ya miaka mingi kuhusiana na mambo yanayohusiana na Taifa hili. Niliwahi kuchangia nikasema without vision people perish pasipo maono watu kuangamia. Mataifa mengi sana yaliyoendelea yana vision ya nchi zao unakuta kwa mfano miaka kama 10 iliyopita Wamarekani walikuwa na a hundred years of the new American wa Finland walikuwa na forty years of the Finland development na nchi nyingine, lakini sisi nchi yetu inakuwa haina vision tulikuwa na Mpango wa Maendeleo wa Mkapa ambao unaisha mwaka 2025.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sasa hivi tuna Ilani za Uchaguzi tu na mipango ya muda mfupi miaka mitano, mipango hiyo inaifanya nchi idumae sana kwanini nasema hivyo, nasema hivyo kwasababu panapokuwa na mpango wa muda mrefu kwa mfano Tanzania tukasema tuwe na mpango wa miaka 50 wa maendeleo na tuna kitu gani tunakiita maendeleo, tunaweza kusema kwa mfano maendeleo kwetu sisi kila mtu awe na maji safi na salama, maendeleo kwetu sisi ndani ya miaka 50 kila nyumba ya mtu iwe na umeme, maendeleo sisi ndani ya miaka 50 asiwepo Mtanzania hata mmoja anayekaa kwenye nyumba ya majani.

Mheshimiwa Naibu Spika, maendeleo kwetu sisi asiwepo Mtanzania kijana mwenye uwezo wa kusoma shule akashindwa kwenda chuo kikuu ndani ya miaka 50, maendeleo kwetu sisi kila barabara iwe ya TARURA iwe barabara ya TANROADS iwe la lami, tukaya-define haya maendeleo kwamba kiongozi anayekuja kwenye power atutimizie hayo maendeleo ndani ya miaka 50 na tutaona ubora wa kiongozi ni kwa jinsi gani anayatimiza hayo maendeleo yetu kwa muda mfupi kuliko muda ambao tumejipangia sisi wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye sera ya Elimu nitakuja kwasababu lengo langu ni kuongea sera ya elimu, lakini shinda inayotusumbua sasa hivi tunahitaji Rais mwenye maono ina maana sisi kama nchi hatuna maono. Kwa hiyo, Rais anapoingia madarakani anatimiza maono yake namna ambavyo yeye anatafsiri maendeleo tunajikuta tunaendelea lakini kwa namna ambavyo kiongozi ana-passive maendeleo, lakini kusema ukweli tusingehitaji Rais mwenye maono tungehitaji nchi yenye maono ili Rais atakapoingia atimize maono ya nchi hayo ambayo sisi wenyewe tumejipangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa mfano kama tungekuwa na maono kwa mfano ndani ya miaka 50 tukasema Wizara ya Elimu tunasema ndani ya miaka 50 tutakuwa na University kila Wilaya, tukasema ndani ya miaka 50 tutakuwa na Hospitali ya Rufaa kila Wilaya kwa hiyo sasa elimu zote zingeanza kujipanga kuelekea hiyo miaka 50. Kwa hiyo, hata wanafunzi wanaosoma wangeiona vision ya nchi, vision ya nchi ni miaka 50 kwa hiyo ndani ya miaka 50 tutakuwa na university kila Wilaya kwa hiyo, kila mtu anayesoma shule angekuwa anajua maprofesa wanatakiwa ma-tutor assistant wanatakiwa, wasomi wanatakiwa kwa hiyo tungemsaidi mwanafunzi kuona mbali kwa sababu ameiona vision ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukisema kwa mfano kwenye miaka 50 kila Wilaya iwe na Hospitali ya Rufaa kwa hiyo anayekwenda shule angeona soko la madaktari lipo nisome madaktari soko la ma-nurse lipo nisome u-nurse anayetaka kuuza vifaa vya medicine angeona naye soko lipo, tungewasaidia hata wawekezaji wetu wakawekeza kwa uzuri zaidi kwasababu wanaiona vision ya nchi, lakini sasa hivi tunakuwa hatuna vision tunakuwa na vitu vya kukimbiza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka huu kwenye Halmashauri yangu kulikuwa na maeneo hakuna madawati wanafunzi wanafaulu tunakimbia kusema tunataka madawati na mwaka kesho tutakimbia tunataka madawati na mwaka kesho kutwa tunataka madawati, kwani hatuna statistics za kujua kwamba mwaka huu estimation za ufaulu zitakuwa kiasi hiki tukaanda madawati, tunakosa vision nikwambie jambo moja Mheshimiwa Waziri kwenye shida yetu tusipoweza ku-handle kuwa na vision kubwa ya Taifa letu maeneo mengi sana tuta-stuck kuna uwekezaji ambao mtu akiwekeza return yake inakuja baadaye sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano ukisema mtu awekeze kwenye kujenga Hospitali ukimaanisha kwamba kutoka kwenye hospitali utapata madaktari kwa hiyo wale wanaosoma wanajua wanakwenda kusoma nitakapofika form six nitachakua medicine kwasababu soko la madaktari lipo anayesoma anasema mimi ninasoma nursing kwasababu madaktari wanatakiwa kila Wilaya soko la nursing lipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanaofanya biashara ya vifaa vya hospitali wataingiza vifaa wanajua ndani ya miaka 50 soko la vifaa vya hospitali lipo. Kwa hiyo hata wale wawekezaji kwenye industry ya elimu wanawekeza wakijua soko lipo. Lakini sasa hivi unasikia wote tumekimbia kwenye gesi baada ya miaka mitatu minne anakuja mwengine gesi haipo, tayari watu wameshajenga hotel wameshajenga nyumba wameshajenga hivi wanakula hasara baadaye kwenye korosho tunapiga kona tena hatuko korosho baadaye kwenye kwenye dhahabu tunapiga kona hapo kwenye dhahabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninawaza nchi hii kama inatakiwa iendelee lazima iwe na vision ya nchi ya muda mrefu ili kiongozi anayeingia ndani ya utawala atumikie vision ambayo wananchi wameiweka sio vision yake. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na mimi kuchangia katika Wizara hii. Kwanza kabisa nimshukuru Mheshimiwa Mashimba Ndaki ambaye ni Waziri wa Wizara hii pamoja na rafiki yangu, Mheshimiwa Abdallah Ulega ambaye ni Naibu Waziri wa Wizara hii. Ingawa siku ya futari ya Waziri Mkuu alisoma Dua mbaya mvua ikanyesha tukashindwa kula vizuri futari, lakini namshukuru hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama Mbunge wa Jimbo la Kawe, jimbo lile limezungukwa na Bahari ya Hindi. Kata za Msasani, Kawe, Kunduchi, Mbweni, Mikocheni na Bunju zote hizi ziko kati ya Bahari ya Hindi na kwa sababu hiyo, kwa uzito sana nalazimika kuchangia hii hoja ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama yalivyo majimbo mengine ambayo yana shughuli kubwa za kilimo, ndivyo ilivyo katika Jimbo la Kawe, shughuli kubwa ya wenyeji wa eneo hilo hasa wale wazawa wanaoishi mwambao wa bahari ni uvuvi. Kwa hiyo, huwezi kuwatenga na uvuvi; ili wale, wanywe, wasomeshe watoto, wajenge nyumba au wafanye shughuli yoyote, maisha yao ni uvuvi. Kwa hiyo ninapojadili kwa habari ya uvuvi kwenye Jimbo la Kawe, ni uti wa mgongo wa wenyeji wa Jimbo la Kawe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, nilipofika ofisini kwake kwa sababu kule Jimbo la Kawe tulikuwa na shida ya uvuvi, wavuvi walikuwa wamezuiwa kutumia ring net wakati wa mchana, kwa hiyo, wavuvi wengi walikuwa wameshindwa kuvua kabisa kwa sababu uvuvi wao wanahitaji kuvua mchana na ili kuvua mchana wanahitaji kutumia ring net.

Mheshimiwa Spika, lakini nikafika kwenye ofisi ya Waziri pamoja na Naibu wake, nikazungumza nao na wakaagiza kwamba wavuvi wote wa Jimbo la Kawe waachwe watumie ring nets mchana wakati Serikali inaendelea kutafakari sheria hiyo na leo wavuvi wangu wanaendelea kufanya vizuri, wanaendelea kuvua murua kabisa, nimshukuru kwa sababu hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni ile sheria ambayo tulijaribu kui-discuss na Naibu Waziri pamoja na Waziri ya kwamba wavuvi wanatakiwa kuvua kwenye mita 50 chini. Mimi ni mdau wa aviation, kwenye aviation kuna kitu kinaitwa transponder ambacho ni chombo chenye uwezo wa kuangalia kina cha maji, nimesafiri siku moja pamoja na meli kutokea Dar es Salaam kwenda Zanzibar tukiwa na chombo hicho kinaitwa transponder ambacho kinaangalia kina cha bahari kutokea kwenye surface ya bahari mpaka chini.

Mheshimiwa Spika, kusafiri kutoka Dar es Salaam mpaka Zanzibar, kina kirefu kuliko chote tulichokipata ni mita 52. Sasa ni ajabu kweli mtu akisema wavuvi wavue kina cha bahari mita 50, maana yake wasafiri kwenda mpaka zaidi ya Zanzibar wakawapate hao samaki, hicho kitu hakiwezekani na kama Waziri akiendelea nacho, basi nitamuondolea shilingi kwenye bajeti yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimshukuru kwa sababu nilipofika ofisini kwake nikajadiliana na yeye akasema kwamba wavuvi waendelee kuvua mahali ambapo wanataka kuvua mpaka hapo Serikali itakapoangalia namna ya kuitengenezea hii sheria mchakato mzuri ili watu waruhusiwe kuvua na wawe na maisha salama zaidi.

Mheshimiwa Spika, nataka nishauri Wizara hii, katika nchi zinazozungukwa na bahari duniani kama ilivyo Japan na nchi zingine, uvuvi pamoja na shughuli za bahari ni ajira kamili inayowasaidia wananchi kupata mapato yao. Kwa mfano, kwenye Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi tumesema kwamba tuta-create ajira milioni nane, na kama Wizara hii itakuwa na ubunifu wa kubuni na kuikuza industry ya uvuvi kwenye maeneo yetu ya Jimbo la Kawe na sehemu zingine, inaweza kuchangia sehemu kubwa sana kwenye kutengeneza ajira za kutosha na kufanya hizi ajira milioni nane zilizoahidiwa na Chama cha Mapinduzi zitokee mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuongeza pato la Taifa, ni muhimu sana kama Serikali ikiwekeza si tu kwenye uvuvi, bali kwenye michezo ya bahari pia na shughuli mbalimbali za bahari na kuitumia bahari sawasawa. Hili linaweza kutusaidia sana kuongeza pato la Taifa na hapo hapo kuwasaidia wavuvi wetu kupata fedha ya kutosha na wakati huo huo kuisadia nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima. Mlipokuwa mkisema kwamba kina kirefu kati ya Dar es Salaam na Zanzibar ni kama mita 50 hivi, nilikuwa naangalia pale juu pale hadi hapa chini, hapa si fifty meters? Haifiki eeh?

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, haifiki hapo, hapo inaweza kuwa 38 hivi. (Kicheko)

SPIKA: Point yangu ni kwamba inaelekea siyo mbali sana, inaelekea Dar es Salaam – Zanzibar kina cha bwawa tu kama la Hombolo pale. (Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nakushukuru kwanza wewe kwa kunipa nafasi ya kuchangia hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa namna anavyofanya kuwasaidia Watanzania. Pia nimshukuru Rais wa Zanzibar, Mheshimiwa Hussein Mwinyi kwa namna anavyofanya kuisaidia Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa ufupi sana mimi nataka kujadili hoja iliyo mezani ya ofisi au hoja ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Nianze kwa kusema maneno haya, kwamba namshukuru sana Mungu, kwamba ninafikiri kuna sababu zinazoifanya nchi yetu ibaki pale ilipo kwa muda mrefu. Sababu mojawapo ambayo nimefikiri sana ni kwamba nchi yetu inahitaji dira au inahitaji ajenda ya taifa au maono ya taifa au mwelekeo wa taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, dunia ina mataifa kama 197 hivi lakini kuna mataifa 193 yanayokubalika na Umoja wa Mataifa. Kwa neema ya Mungu mimi nimewahi kufika zaidi ya mataifa 143, ni mataifa hamsini tu ya duniani ambayo sijawahi kufika. Lakini mshangao ambao nimekuwa nao sana kwa miaka mingi ni kwamba mataifa yote yenye watu wa asili ya Afrika, kwa maana ya ngozi yetu yanaasili za kufanana yana matatizo yanayofanana na yapo nyuma kwa aina ya kufanana. Suala hili limenifanya nijiulize sana kwa nini mataifa yenye asili ya watu wa Afrika wheather Latin America, or Afro- Caribbean kwa maana ya Jamaica Hyatt na mengine yana matatizo yanayofanana?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo moja nikaligundua juu ya mataifa haya; kwamba mataifa haya hayana maono ya muda mrefu yanayoifanya nchi iwe guided kiasi kwamba kila utawala unapoingia katika mamlaka ufuate maono ya muda mrefu. Simaanishi kwamba hakuna maono kabisa, lakini hebu nitoe mfano kidogo. United Arab Emirates wana mpango wa kuanzia mwaka 2050 mpaka 2117 wa kuhamishia makazi ya kwanza katika Sayari ya Mars, ni mpango wa taifa wa muda mrefu. Lakini pia United Arab Emirates wana mpango wa kuwa nchi ya kwanza duniani katika nchi 10 zenye hifadhi ya chakula cha kutosha kufikia mwaka 2051. Vilevile, United Arab Emirates wana Mpango wa Taifa wa Clean Energy kuanzia 2020 mpaka 2030. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hakuna taifa lililoendelea duniani bila mpango wa muda mrefu. Tusipokuwa na mpango wa muda mrefu kasi ya maendeleo haitaenda kama inavyotakiwa. Niliwaza kwamba inawezekana labda tunashindwa kupanga mpango wa muda mrefu kwa sababu labda katiba haituruhusu au sheria haituruhusu. Nikasoma Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 63 (3)(c) inasema hivi: -

(3) Kwa madhumuni ya utekelezaji wa madaraka yake -

(c) kujadili na kuidhinisha mpango wowote wa muda mrefu au muda mfupi unaokusudiwa kutekelezwa katika Jamhuri hii ya Muungano, na kutunga sheria ya kusimamia utekelezaji wa mpango huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikaona kumbe katiba yetu inaruhusu, kwamba Serikali inaweza kuleta mpango wa muda mrefu wa namna ambavyo Tanzania iwe miaka 50 ijayo, Tanzania iwe miaka 80 ijayo ili kila utawala unaoingia madarakani ufuate maono ya nchi ambayo nchi imejipangia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hatari itatupata siku zijazo. Kwamba, ndiyo maana unasikia watu wanasema tunahitaji Rais mwenye maono, tunahitaji Rais mwenye maono kwa sababu nchi haina maono, tunahitaji nchi yenye maono ili kila Rais anayeingia madarakani afate maono ya nchi tuliyoiweka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutaruhusu kila mtu anayeingia madarakani aongozwe na kichwa chake anavyowaza yeye kuna siku tutapata Rais wa ajabu tutadondokea pua hatutaamini macho yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unakumbuka vizuri baada ya vita vya pili vya dunia nchi za ulaya zilifilisika kabisa. Ukiangalia Wa-Marekani wakaanza mpango unaoitwa marshal plan, marshal plan kipindi kile Rais wa Marekani alikuwa Truman, wakaanza mpango wa kuzisaidia nchi 17 za ulaya magharibi zilizokuwa zimefirisika kabisa. Nchi hizo wakazipa almost dola bilioni 13 ambayo ni bilioni 115 kwa sasa. Marekani akawaambia kila nchi izalishe mpango wake wa muda mrefu na dira yake. Kila nchi ikazalisha dira yake, mpango wake na zikapewa hizo fedha; nan chi hizo zikatoka hazipo kama sisi tulivyo. Sisi mpango tulionao sasa ni kufikia tu 2026.

Mheshimiwa Naibu Spika, maombi yangu ni kwamba tuipe dira nchi yetu, tuwe na mpango wa zaidi ya miaka 50 au miaka 60 au miaka 100 ya Tanzania ijayo ili mitaala yote ya shule na ilani zote za chaguzi na watoto wote waweze kuiona Tanzania kwenye three D na waweze kujifunza na kuiona Tanzania ijayo; vinginevyo tutapoteza muda mwingi sana kwa kuzunguka pale pale na kufanya mambo yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikupe mfano; tumekuwa na regime iliyopita ilifanya vizuri sana. Tumekuwa na Rais wetu Mwalimu Nyerere aliendelea kwa namna yake akaja Mwinyi aliendelea kwa namna yake, lakini alipoishia Nyerere, Mheshimiwa Mwinyi hajaendelea pale, alipoishia Mwinyi, Mkapa hajaendelea pale, alipoishia Mkapa, Kikwete hajaendelea pale, alipoishia Kikwete, Magufuli hajaendelea pale tunakuwa kila Rais anayeingia madarakani anaanza chake na matokeo yake tutapata Rais wa ajabu tutaangukia pua hujawaji kuona. There is no country that can develop within a single regime, nchi zote zinazoendelea ni mwendelezo wa regime ya kwanza, regime ya pili, regime ya tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ili regime ibaki kwenye guidance lazima yawepo maono ya taifa ili Rais anayeingia madarakani ayatumikie maono ya taifa na sisi wananchi tuyaone kama maono ya taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima tu-define ni kitu gani sisi tunakiita maendeleo, tunachokiita maendeleo sisi si lazima kiitwe maendeleo Marekani. Kwa mfano; tunaweza kuwa na namna yetu ya kusema kwetu sisi maendeleo …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gwajima sekunde tatu malizia.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: …kwetu sisi maendeleo kila mtu awe na maji safi, kwetu sisi maendeleo tuwe na hospitali. Kwa hiyo, ninaomba kusema ni muhimu sana nchi yetu iwe na Dira ya Taifa na Maendeleo ya Taifa ili kila Rais anayeingia madarakani awe mzuri awe wa namna gani asimamie maono ya nchi tuliyoyaweka na wala si maono yake mwenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie katika hoja hii iliyopo mbele yetu. Kwanza ninakushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii lakini kwa maksudi ya kuokoa wakati, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa bidii yake anayoifanya kutusimamia Watanzania na kuhakikisha ndoto ya Watanzania inatimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nichukue nafasi hii kuwashukuru vijana wa kutoka Jimbo la Kawe, Kata ya Mabwepande ambao vijana hawa walitembea kwa mguu kutokea Dar es Salaam mpaka Bukoba kwa kusudi la kum- support Mheshimiwa Rais katika juhudi zake. Shukurani zangu ni kubwa sana kwao kwa sababu wametembea kilometa 1,382 kwa siku 35. Wakati wana wa Israel walipokuwa wanatoka katika nchi ya Misri, walisafiri kilometa 405 kwa miaka 40, lakini hawa vijana wamesafiri kilometa 1,382 kwa siku 35, hawa ndiyo mashajaa wa Jimbo la Kawe. Vijana hao ni Abiudi Maugo, Alinda Albert, Saidi Apollo, Idrissa Rajabu, Mossi Fikiri, Kassim Kidole na Bura William, nawashukuru sana hawa vijana wa Jimbo la Kawe.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Nitachangia mchango huu tena na tena mpaka Yesu Kristo atakaporudi tena kama haijafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka ieleweke kwamba, Friction au msuguano ni sehemu mojawapo ya ujenzi, na tujue kwamba msuguano au friction ndio ulileta ufumbuzi wa kwanza wa moto. Kutofautiana kimawazo ni jambo la kawaida kama lengo lenu ni kujenga nyumba moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaza kwamba pamoja na mpango mzuri ambao Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango aliuwasilisha lakini tunahitaji Mpango wa muda mrefu. Nataka nikubaliane na Mheshimiwa Shabiby aliyechangia jana, kwamba hakuna nchi duniani, narudia tena there is no country on global ambayo imeweza kuwavusha watu wake au kuleta maendeleo kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zote ambazo zimevusha watu wao zilikuwa na mipango ya muda mrefu na zikaisimamia. Kwa mfano tunakumbuka baada ya vita vya kwanza vya dunia, nchi za Ulaya zote zilifilisika; ni kwa sababu tu Marekeni haikupigana vita hivyo katika nchi yake; lakini zaidi ya nchi 16 Ulaya zilifilisika na zilikuwa zimekwisha kabisa kiuchumi. Kipindi kile alikuwepo Rais wa Marekani anaitwa Truman na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje George Marshall akaweka mpango wa kuziokoa nchi
16 za Ulaya kiuchumi na zikapewa fedha. Na katika mpango wake zikaambiwa kwanza ziandae Mpango wa Maendeleo wa muda mrefu. Nchi zile zikaanda Mpango wa Maendeleo wa muda mrefu katika nchi 16 za Ulaya, ikiwemo Ujerumani na Swaziland.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maandalizi yake ya Mpango wa muda mrefu na fedha zilizopata kutokea Marekani wakavusha nchi zao mpaka leo ni nchi za ulimwengu wa tatu, zilikuwa zimefilisika kabisa. Ukimwona mwenzako anatumia farasi fulani wa kumkimbiza kwenda kwenye hatma na wewe ukimtumia farasi huyo huyo atakufikisha kwenye hatma hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashangaa kwa nini sisi pamoja na mipango mizuri ya mwaka mmoja, miaka mitano tunashindwa nini kuwa na mipango ya muda mrefu miaka 60 ya maendeleo ya Tanzania au miaka 70 ya maendeleo ya Tanzania na hii mipango ikavunjwa kwenye vipande vidogovidogo kwa malengo ya kuitimiza. Kwa mfano tumejenga SGR ni jambo zuri na ni safi kabisa. Lengo la SGR ni kwamba tubebe mzigo wa kutosha ili tuiongezee nchi yetu kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mzigo unatokea wapi? Mzigo unatokea bandarini. Kwa hiyo lakini bandari haijapanuliwa bado; tumeanza na SGR na bandari bado ile ile. Kwa hiyo kama tungekuwa na mipango tungekuwa tumeanza kupanua bandari kwanza ili kusudi hii bandari SGR itakapokamilika tuweze kubeba mzigo mkubwa tuupeleke mpaka Kigoma na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa unaona ukweli wenyewe kwamba SGR inaelekea Kigoma, Bandari ya Dar es Salaam ni hiyo hiyo, tumehamia tena Bandari ya Bagamoyo mahala ambapo SGR haipo. Kitakacholazimisha kufanyika tena itabidi tujenge kipande kingine cha kutokea Bagamoyo kwenda kuunga kwenye SGR ili tuwe na uwezo wa kubeba mizigo mikubwa na kuiongezea uchumi nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili lisingekuwepo kama tuna mipango. Wakati huo huo hii mizigo mingi ambayo tunataka tubebe inaelekea wapi? tunakwenda mpaka Kigoma tuivushe kwenda Congo. Je, tumeshajiandaa kuivusha mizigo hiyo kutokea Kigoma ama kwa njia ya Ziwa Tanganyika kwenda Congo? Hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya muda mrefu ya nchi ndiyo njia peke yake ambazo nchi zilizoendelea zilitumia kuzitoa nchi zao zilipokuwa na kuzipeleka mahala ambapo nchi hizi zilikwenda. Nitoe mfano mwingine, ya kukufanya Mheshimiwa Mwenyekiti na Wabunge wenzangu kuwafikirisha, kwa mfano tumejenga Stigler’s Gorge mahala ambapo tutazalisha umeme mwingi ni jambo zuri kwa sababu power ndiyo njia pekee ya kuifanya nchi ijenge viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango wa kujenga Stigler’s Gorge hatukupanga ule umeme tutautoaje hapo Stigler’s Gorge kuingia kwenye gridi ya Taifa. Mtu yeyote ambaye ni genuine nimuulize, je, wakati mnapanga ujenzi wa Stigler’s Gorge je, kuna bajeti ya kutoa umeme pale Stigler’s kuingiza kwenye gridi ya Taifa mpango haukuwepo. Hii ni kuonesha kwamba, nasema sisi simlaumu mtu, ni kuonesha kwamba matatizo yetu yanatokana na kukosa mipango ya muda mrefu. Tunapopanga mipango ya muda mfupi there is no country on the global will ever develop kwa kuwa na mipango ya muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja ambalo linaweza likamgusa mtu lakini sio kwa ubaya. Ili nchi iendelee haihitaji tu natural resources, hapana, nchi kwa mfano Sweden, Denmark, Sweden wanatengeneza scania hawahimbi chuma kama cha kwetu. Japan ndio supplier wa magari, iron ya Japan ilikwisha muda mrefu wanaagiza chuma kutoka Australia. Ni mipango tu wanayofanya. Lakini sisi tuna natural resources za kutosha ila ile akili ya kugeuza natural resources kuwa maisha ya wananchi ndiyo hiyo tunapungukiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri, namwita Mheshimiwa Festo Sanga ajiandae Mheshimiwa Asha…

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami nichangie katika hoja hii iliyopo mbele yetu. Kwanza ninakushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii lakini kwa maksudi ya kuokoa wakati, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa bidii yake anayoifanya kutusimamia Watanzania na kuhakikisha ndoto ya Watanzania inatimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nichukue nafasi hii kuwashukuru vijana wa kutoka Jimbo la Kawe, Kata ya Mabwepande ambao vijana hawa walitembea kwa mguu kutokea Dar es Salaam mpaka Bukoba kwa kusudi la kum- support Mheshimiwa Rais katika juhudi zake. Shukurani zangu ni kubwa sana kwao kwa sababu wametembea kilometa 1,382 kwa siku 35. Wakati wana wa Israel walipokuwa wanatoka katika nchi ya Misri, walisafiri kilometa 405 kwa miaka 40, lakini hawa vijana wamesafiri kilometa 1,382 kwa siku 35, hawa ndiyo mashajaa wa Jimbo la Kawe. Vijana hao ni Abiudi Maugo, Alinda Albert, Saidi Apollo, Idrissa Rajabu, Mossi Fikiri, Kassim Kidole na Bura William, nawashukuru sana hawa vijana wa Jimbo la Kawe.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuchangia hoja iliyo mbele yetu. Nitachangia mchango huu tena na tena mpaka Yesu Kristo atakaporudi tena kama haijafanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka ieleweke kwamba, Friction au msuguano ni sehemu mojawapo ya ujenzi, na tujue kwamba msuguano au friction ndio ulileta ufumbuzi wa kwanza wa moto. Kutofautiana kimawazo ni jambo la kawaida kama lengo lenu ni kujenga nyumba moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaza kwamba pamoja na mpango mzuri ambao Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango aliuwasilisha lakini tunahitaji Mpango wa muda mrefu. Nataka nikubaliane na Mheshimiwa Shabiby aliyechangia jana, kwamba hakuna nchi duniani, narudia tena there is no country on global ambayo imeweza kuwavusha watu wake au kuleta maendeleo kwa muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi zote ambazo zimevusha watu wao zilikuwa na mipango ya muda mrefu na zikaisimamia. Kwa mfano tunakumbuka baada ya vita vya kwanza vya dunia, nchi za Ulaya zote zilifilisika; ni kwa sababu tu Marekeni haikupigana vita hivyo katika nchi yake; lakini zaidi ya nchi 16 Ulaya zilifilisika na zilikuwa zimekwisha kabisa kiuchumi. Kipindi kile alikuwepo Rais wa Marekani anaitwa Truman na Waziri wa Mambo ya Nchi za Nje George Marshall akaweka mpango wa kuziokoa nchi
16 za Ulaya kiuchumi na zikapewa fedha. Na katika mpango wake zikaambiwa kwanza ziandae Mpango wa Maendeleo wa muda mrefu. Nchi zile zikaanda Mpango wa Maendeleo wa muda mrefu katika nchi 16 za Ulaya, ikiwemo Ujerumani na Swaziland.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maandalizi yake ya Mpango wa muda mrefu na fedha zilizopata kutokea Marekani wakavusha nchi zao mpaka leo ni nchi za ulimwengu wa tatu, zilikuwa zimefilisika kabisa. Ukimwona mwenzako anatumia farasi fulani wa kumkimbiza kwenda kwenye hatma na wewe ukimtumia farasi huyo huyo atakufikisha kwenye hatma hiyo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashangaa kwa nini sisi pamoja na mipango mizuri ya mwaka mmoja, miaka mitano tunashindwa nini kuwa na mipango ya muda mrefu miaka 60 ya maendeleo ya Tanzania au miaka 70 ya maendeleo ya Tanzania na hii mipango ikavunjwa kwenye vipande vidogovidogo kwa malengo ya kuitimiza. Kwa mfano tumejenga SGR ni jambo zuri na ni safi kabisa. Lengo la SGR ni kwamba tubebe mzigo wa kutosha ili tuiongezee nchi yetu kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mzigo unatokea wapi? Mzigo unatokea bandarini. Kwa hiyo lakini bandari haijapanuliwa bado; tumeanza na SGR na bandari bado ile ile. Kwa hiyo kama tungekuwa na mipango tungekuwa tumeanza kupanua bandari kwanza ili kusudi hii bandari SGR itakapokamilika tuweze kubeba mzigo mkubwa tuupeleke mpaka Kigoma na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa unaona ukweli wenyewe kwamba SGR inaelekea Kigoma, Bandari ya Dar es Salaam ni hiyo hiyo, tumehamia tena Bandari ya Bagamoyo mahala ambapo SGR haipo. Kitakacholazimisha kufanyika tena itabidi tujenge kipande kingine cha kutokea Bagamoyo kwenda kuunga kwenye SGR ili tuwe na uwezo wa kubeba mizigo mikubwa na kuiongezea uchumi nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili lisingekuwepo kama tuna mipango. Wakati huo huo hii mizigo mingi ambayo tunataka tubebe inaelekea wapi? tunakwenda mpaka Kigoma tuivushe kwenda Congo. Je, tumeshajiandaa kuivusha mizigo hiyo kutokea Kigoma ama kwa njia ya Ziwa Tanganyika kwenda Congo? Hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya muda mrefu ya nchi ndiyo njia peke yake ambazo nchi zilizoendelea zilitumia kuzitoa nchi zao zilipokuwa na kuzipeleka mahala ambapo nchi hizi zilikwenda. Nitoe mfano mwingine, ya kukufanya Mheshimiwa Mwenyekiti na Wabunge wenzangu kuwafikirisha, kwa mfano tumejenga Stigler’s Gorge mahala ambapo tutazalisha umeme mwingi ni jambo zuri kwa sababu power ndiyo njia pekee ya kuifanya nchi ijenge viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango wa kujenga Stigler’s Gorge hatukupanga ule umeme tutautoaje hapo Stigler’s Gorge kuingia kwenye gridi ya Taifa. Mtu yeyote ambaye ni genuine nimuulize, je, wakati mnapanga ujenzi wa Stigler’s Gorge je, kuna bajeti ya kutoa umeme pale Stigler’s kuingiza kwenye gridi ya Taifa mpango haukuwepo. Hii ni kuonesha kwamba, nasema sisi simlaumu mtu, ni kuonesha kwamba matatizo yetu yanatokana na kukosa mipango ya muda mrefu. Tunapopanga mipango ya muda mfupi there is no country on the global will ever develop kwa kuwa na mipango ya muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme jambo moja ambalo linaweza likamgusa mtu lakini sio kwa ubaya. Ili nchi iendelee haihitaji tu natural resources, hapana, nchi kwa mfano Sweden, Denmark, Sweden wanatengeneza scania hawahimbi chuma kama cha kwetu. Japan ndio supplier wa magari, iron ya Japan ilikwisha muda mrefu wanaagiza chuma kutoka Australia. Ni mipango tu wanayofanya. Lakini sisi tuna natural resources za kutosha ila ile akili ya kugeuza natural resources kuwa maisha ya wananchi ndiyo hiyo tunapungukiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante kwa mchango mzuri, namwita Mheshimiwa Festo Sanga ajiandae Mheshimiwa Asha…

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi nichangie katika hoja hizi mbili, kwa maana ya hoja ya Kamati ya Kilimo, Uvuvi na Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu. Mimi kwa sababu ya muda nitaongelea hoja mojawapo tu hii hoja ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu.

Mheshimiwa Spika, Kamati hii imefanya kazi nzuri sana kwa sababu Kamati hii inaishauri Serikali kwa niaba ya Wabunge wote. Katika ushauri wake kwenye maoni na mapendekezo ya Kamati, kuna mahala Kamati hii imesema categorically kwamba, sababu mojawapo ya kwa nini miradi mingine ya Serikali inashindwa kutimia ni sababu ya ufinyu wa bajeti ya baadhi ya taasisi. Imetoa mfano mojawapo kama TANROADS.

Mheshimiwa Spika, napenda kuongezea kwenye ushauri ambao Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu imeshauri. Kwa mfano, tunafahamu vizuri kabisa duniani kwamba resources are limited but needs are unlimited. Kwamba vyanzo vina ukomo lakini mahitaji hayana ukomo. Kwa hiyo ni ushauri wangu kwamba, Wizara hii inapokuwa inapanga taratibu zake za ujenzi wa barabara iwe inatumia Kanuni ambayo tunaita Kanuni ya kipaumbele au the principle of priority.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano kwenye Kanuni ya kipaumbele, kwamba resources are very limited but needs are unlimited. Kwamba tunakuwa na vyanzo vilevile lakini mahitaji ni mengi kuliko vyanzo, kwa hiyo lazima uwe na sheria ya kutoa kipaumbele uanze na nini, umalizie na nini kutegemea na umuhimu wake kwa wakati wake. Kwa mfano, kuna barabara inayotoka Tegeta inapanda mpaka Kiwanda cha Wazo Hill - Kiwanda cha Cement mahala ambapo, ni barabara ina urefu kama wa kilomita Tatu au Nne hivi. Kama unavyojua kiwanda hiki cha Wazo Hill kilijengwa tangu 1966. Wakati kiwanda hiki kinajengwa wananchi walikuwa hawakai hayo maeneo ya Tegeta, maeneo ya Madale lakini sasa kiwanda kimejengwa na wananchi wanakaa, barabara hii ni nyembamba kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unapojaribu kujiuliza ni kwa nini hii barabara haijajengwa? Nikupe takwimu za kweli kutoka kiwandani. Kiwanda hiki kinatoa corporate tax kwa mwaka zaidi ya Bilioni 100, narudia tena Bilioni 100 corporate tax kwa mwaka, lakini barabara yake ni nyembamba kiasi kwamba mwaka huu tu tulioumaliza 2022 zaidi ya watu 10 wameuawa pale kwa ajali kwa sababu barabara ni nyembamba malori yanapangana kutoka kiwandani kuja pale Tegeta na yanasababisha ajali si za kawaida.

Mheshimiwa Spika, sasa unaweza kujiuliza, kama kiwanda hiki kinaipa Serikali ushuru Bilioni 100 corporate tax kwa mwaka, kuna tatizo gani kwa Serikali kupanua barabara hii ili malori yatembee na ipate ushuru zaidi. It’s very simple principle kwamba huyu ng’ombe ambaye anakupa maziwa, unampa majani ya kutosha ili upate maziwa zaidi ununue ng’ombe wengine. Lakini kwa kutokujua kanuni ya priority ni kwamba barabara hiyo haijajengwa, matokeo yake malori yanapangana kutoka Tegeta kiwandani yanafika pale mpaka Tegeta barabarani hayawezi kwenda. Kumbe kama tungeweza kupanua barabara hii kwa kuangalia priority hawa watu wanaotulipa Bilioni 100 kwa mwaka wangekuwa wana uwezo wa kulipa zaidi ya pale na tungejenga barabara nyingine zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi naishauri Serikali kwamba, it is very important and crucial kuwa tunaangalia priority tuanze na nini ili kitupe nini kwa ajili ya kujenga mahali pengine, hili ni jambo la muhimu sana. Inashangaza kwamba imekuwa kero kubwa sana kwa watu wa pale kwa sababu watu wanauwawa kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo jingine la kuangalia ni muhimu sana TANROADS au na Wizara hii wakati wanapanga bajeti zao waangalie priority. Kwa mfano, kuna bandari moja pale Mbweni barabara ya kwenda kwenye Bandari ya Mbweni, bandari ndogo mahali ambapo watu wanafanya biashara kati ya Zanzibar na Mbweni. Bandari ile ni ndogo tu lakini kwa mwezi inakusanya mapato Milioni 400, lakini ile barabara tu ya kwenda bandarini haipo kiasi kwamba watu wanatumiwa ng’ombe. Yaani Mashekhe wangu pale lazima watumie ng’ombe kubeba mizigo yao. Can you imagine Dar es Salaam - Mbweni mahali ambapo Milioni 400 zinakusanywa kila mwezi, hakuna barabara ya kufika kwenye bandari hiyo lazima watu wabebe na ng’ombe, hizi milioni 400 zinaenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilikuwa nafikiri it is very crucial kutumia kanuni ya kipaumbele (the principle of priority) kwamba mahali panapozalisha tupatengenezee barabara ili pazalishe zaidi kwa ajili ya fedha za kuisaidia nchi yetu, hii it is a simple mathematics it doesn’t cost matrix, haihitaji matrix wala integration. Kwamba hapa wanalipa milioni 400 kwa mwezi lakini hawana barabara, gari haiwezi kufika bandarini, wanatumia ng’ombe ukifika pale ni Dar es Salaam lakini kwenda pale bandarini lazima utumie ng’ombe. Sasa kama wangekuwa wametumia magari tungezalisha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo naomba sana kujaribu kuunga huu ushauri na Kamati ya Miundombinu kwamba ni muhimu sana kuangalia priority waanzie wapi ili tupate nini kwa ajili ya kupata nini pale baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee na palepale kuionesha Wizara hii kwamba wakitumia the principle of priority itawasaidia sana. Kwa mfano, pale Basihaya kuna mtaro wa maji, huu mtaro wa maji, maji huwa yanajaa yanaporomoka kutoka juu yanaua watu kila mwaka. Kila mwaka watu wanauawa kwa sababu ya mtaro wa Basihaya mpaka Nyamachabes. Serikali ilishafanya tayari study pale kuonesha kwamba TANROADS wanatakiwa kujenga mtaro wa ku-deliver maji kwenda baharini.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alipopita pale aliahidi akasema mtaro huu utajengwa. Haya sasa siyo maendeleo, haya ni kuokoa maisha ya watu wanaoangamia kwa ajili ya mafuriko wakati wa mvua. Inashangaza sana, unakuta eneo lile lilikuwa na tatizo la maji kwa maana kwamba watu hawana maji, wakati huo huo lina tatizo la mafuriko ukimwelezea mtu hawezi kukuelewa. Una tatizo la upungufu wa maji, wakati huo huo una tatizo la mafuriko anakwambia akili yako ina matatizo. Hii ni kwa sababu ya kutokujua priorities, tuanze na nini, tufuate na nini ili tupate nini hapo baadae. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie tu bila kuchukua muda wako mwingi kwamba ni muhimu sana hii Kamati ya Miundombinu imeshauri jambo zuri kwamba Serikali ni vizuri sana iweke priorities mahali ambapo panatupa return kubwa tuwekeze zaidi ili tupate return ya kutosha kwa ajili ya kuijenga nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kwenye hilo hilo. Kuna barabara inayotoka Bunju ‘B’ kwenda Mabwepande inaenda mpaka Kihonzile, inakwenda kuunga mpaka ile barabara ya stendi ya Mbezi mwisho. Ukiangalia kwenye priorities hizo hizo kwamba Wizara hiyo inafanya priority barabara hiyo inatokea Mbezi Luis inakuja kwenye Jimbo la Kawe kupita Mabwepande mpaka Bunju B. Ingejengwa ungeona badala ya mabasi kutoka Morogoro yakaingia Ubungo Mjini yangekuwa yanapita moja kwa moja yanatokea Mabwepande na hata ile maana ya kujenga Bandari ya Bagamoyo mtu angetoka kule aka-connect moja kwa moja kwenda Morogoro. Kwa hiyo ni muhimu sana Wizara ichukue ushauri wa Bunge kwamba tuangalie priority tunapofanya mambo yetu kwa sababu resources are limited but needs are unlimited.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikusukuru sana wewe binafsi kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hoja hii ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru Mheshimiwa Rais ambaye kwa logic hasa na yeye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini pia ni Waziri wa hii ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujikita hasa kuongea kwa Habari ya dhana ya utawala bora. Mwaka jana siku kama hii wakati hoja ya ofisi hii imeletwa mezani niliomba Serikali kupitia aliyekuwa Waziri, Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa, kwa Habari ya Masheikh wa Uamsho waliokuwa wamekaa miaka minane jela bila kupelekwa Mahakamani. Na nilipoiomba Serikali, naishukuru Serikali kwamba, ilifanyia kazi vizuri na Masheikh hawa waliachiwa. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiri, pia niliomba tena Serikali kwa ajili ya kutekeleza dhana ya utawala bora wakati ule, kushughulika na suala la Mashekhe waliokuwa Arusha. Masheikh zaidi ya 18 ambao nao waliwekwa ndani miaka mingi bila kesi yao kusikilizwa, nashukuru Serikali imeyatimiza hayo na Mashekhe hao waliachiwa ahsante sana nakushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo liko jambo moja tu ambalo nataka kulizungumzia leo ambalo ni dhana ya utawala bora. Mara nyingi Viongozi Wakuu kama Rais, wanapotoa matamko yenye lengo la kuijenga nchi, viongozi walio chini ambao ni wajibu wao kutekeleza matamko hayo, wanatakiwa wawe makini sana na mahiri sana katika kuyatekeleza matamko ambayo yametolewa na Viongozi Wakuu kama Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano nimnukuu Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan katika mkutano wake mmoja alisema: “ninaomba muwapange wamachinga” hayo ndiyo maneno aliyosema, hakusema naomba muwafukuze wamachinga, hakusema naomba muwapige wamachinga, hakusema naomba muwavuruge wamachinga. Mheshimiwa Rais alisema naomba muwapange wamachinga. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili lilileta mambo ya ajabu, dhana ya Mheshimiwa Rais iwapange wamachinga ilikuwa njema, nzuri yenye maana na tija kwa wamachinga wenyewe. Lakini watekelezaji walipoanza kutekeleza dhana hii, wakaanza kuwakimbiza wamachinga kuwapiga, kuwanyang’anya mali zao, bomoa mabanda yao, haikuwa dhana ya Mheshimiwa Rais na hii inaharibu dhana ya ujumla ya utawala bora kwa wale watekelezaji walio chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano, Mheshimiwa Rais aliposema wapangeni wamachinga hakumaanisha wafukuzwe. Kupanga wamachinga siyo lazima uwaburuze ukawaweke kwenye kibanda, dhana ya machinga anamfata mteja, machinga hafuatwi na mteja hiyo ndiyo dhana ya machinga. Ukimchukua machinga ukamuweka kwenye kona siyo machinga tena, ukamuweka kwenye duka siyo machinga tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano tena, sehemu kama Uingereza kwa mfano ukienda Tottenham au East London kuna nyakati ambazo wanafunga mitaa kuwaruhusu wale vendors wauze vitu vyao, hata wakati fulani hapa wakati wa utawala wa Mzee Kikwete ile barabara yetu ya karibu na Makao Makuu ya Chama cha Mapinduzi Jumamosi walikuwa wanafunga ili hawa watu wauze vitu vyao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea Watendaji wenye akili yenye kupanga vizuri, wangewaza badala ya kuwafukuza wamachinga wawe angalau na machinga’s day, waseme wamachinga fanyeni kazi yenu Jumatatu au fanyeni kazi yenu Jumanne au Jumatano kuwe na siku moja wapo ambayo wamachinga wanaruhusiwa kufanyakazi zao ili kuruhusu utaratibu mwingine uendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifanya kama ulivyofanya kwa wamachinga leo, nakuhakikishia wamachinga watarudi tena mitaani kama kawaida. Huwezi kuwaweka kwenye banda wamachinga na ukafikiri watakaa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, halafu hawa machingas ni fans wetu wakubwa wa uchaguzi na ndiyo wapiga kura wetu wakubwa sana tunapowavuruga leo watatuvuruga siku chache zijazo, tutavurugika kweli kweli na tusijifanye hatuoni. Kuna msomi mmoja aliwahi kusema ni afadhali kisu cha Daktari kinachopasua ngozi kwa lengo la kuponya, kuliko dawa ya kuondoa maumivu inayomponya mtu kwa muda halafu ikampeleka kwenye maumivu ya kifo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tuseme ukweli, kwenye suala la machinga we are on the wrong destination, tumeenda vibaya na wamachinga hawa watatuhukumu siku chache zijazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa kwenye Kata ya Kawe, Mikocheni, Bunju na maeneo mengine ya Jimbo la Kawe nina wamachinga wa kutosha, ninaomba nijitoe kabisa kwenye hili suala la kuwakimbiza wamachinga na kuwapeleka kona moja baada ya nyingine kwa mambo ambayo wangeweza kutengenezewa na wakakaa vizuri na wakaenda vizuri. Kwa hiyo, hapa hatujaenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nisema kuna baadhi ya watu wanamharibia Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais alikuwa na maana njema kabisa, wapangwe wamachinga! Kupangwa angesema wamachinga fanyeni shughuli zenu za machinga Alhamis peke yake, siku zingine mtulie nyumbani, hiyo ndiyo maana ya kupanga wamachinga. Huwezi kusema wamachinga wajipange wakati ni watu wenye njaa wanahitaji chakula, after all kusema ukweli hatuwezi kufikia mpangilio kwa viwango vya Ulaya, hii vurugu mechi yetu ya wamachinga ndiyo utalii wenyewe ule kwetu huku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii mismatch ya machinga ndiyo yenyewe. Kwa hiyo, nataka kusema hapa hatujaenda sawa na lazima tujue lile soko la Ilala Machinga litengenezwe halina machinga mle sasa hivi, tunatengeneza masoko mengine ya machinga hayatakuwa na matching guys wataendelea kuzurura mitaani, kwa hiyo lazima tuwe na namna nzuri ya kuwa handle hawa mabwana kwa sababu nao ni Watanzania wenzetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho...

MWENYEKITI: Naomba utumie dakika moja kuhitimisha Mheshimiwa Gwajima.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, dakika zangu zimekimbia haraka. Naomba sasa nihitimishe kwa kusema ni vizuri viongozi wetu wakubwa wanapotoa maelekezo, watekelezaji walio chini waangalie modality nzuri ya kutekeleza hayo yaliyosemwa na kiongozi ili kuondoa kumfanya kiongozi aonekane ameharibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nami nikushukuru sana wewe binafsi kwa kunipa nafasi kuchangia hii hoja iliyoko mbele yetu, ya Wizara ya Uvuvi na Ufugaji. Pia namshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa bidii yake anayofanya katika kuhakikisha Taifa la Tanzania linajengwa na linabaki salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia namshukuru Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ujasiri wake wa kumchagua ndugu yangu Mheshimiwa Ulega pamoja na ndugu yake Mheshimiwa David Silinde kuwa Mawaziri wenye dhamana kwa Wizara hii. Hongereni sana. We have so many good Ministers, and you are one of them. Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, napenda kumpongeza Mheshimiwa Kitandula kwenye mchango wake pamoja na Mheshimiwa Kaijage na Mheshimiwa Mathayo, Mbunge wa Musoma Mjini. Nikuhakikishie Waziri mwenye dhamana ya mifugo pamoja na uvuvi, mimi sitakuondolea Shilingi na ninaunga mkono hoja yako kabla sijaendelea. Nafahamu kwamba umeomba Shilingi bilioni 295.9, hizo sina neno nazo, na nitakupa na akili nyingine ya kupata zaidi ya hapo. Ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichokoze jambo. Kwenye document ya mtani wangu, Mheshimiwa Waziri Ulega, kwa niaba ya Serikali, ametuonesha kwamba, sekta ya uvuvi inachangia asilimia moja ya pato la Taifa. Hili jambo ni hatari sana kulisikia au kusemwa mbele ya watu wenye akili timamu. Nichokoze jambo ambalo litamfanya kila mtu afikiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ukianzia kwenye maji ya chumvi; tuna mikoa ambayo imezungukwa na maji ya chumvi. Kwanza ni Dar es Salaam, Mkoa wa Pwani, Mkoa wa Lindi, Mkoa wa Mtwara, Mkoa wa Tanga na Zanzibar yote. Hii ni mikoa almost mitano pamoja na Zanzibar, yote imezungukwa na maji. Ukiamua kuangalia maziwa tuliyonayo, tunayo mikoa ambayo na yenyewe imezungukwa na maji ya maziwa, siyo kwa maana ya maziwa ya kunywa, ni kwa maana ya lakes. Mkoa wa Mwanza umezungukwa na maji, Mkoa wa Mara, Mkoa wa Simiyu, Geita, Kagera, Mbeya, Kigoma, Katavi, Rukwa, Ruvuma, Arusha kuna Natron, mpaka kuna Ziwa Jipe Kilimanjaro, kuna Manyara, mpaka kwa Wagogo hapa kuna Mtera, tumezungukwa na maji mpaka Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukijaribu kuunganisha hizi dots za hii mikoa 16 niliyoitaja yote iko kando ya maziwa. Unaunganisha na hii mikoa mingine niliyoitaja ambayo iko kando ya maji ya chumvi, unakuta mikoa 22 yote imezungukwa na maji. Sasa kwa akili ya kawaida, it doesn’t hold water kugundua kwamba liko tatizo tunaloli-face ambalo tunahitaji kulitatua kwa pamoja ili kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijaribu kufanya troubleshooting kidogo. Kwanza, haikubaliki kwa namna yoyote ile kwamba uvuvi uchangie asilimia moja peke yake kwenye pato la Taifa, haiwezekani ukilinganisha na resources tulizonazo. Sasa ushauri wangu wa kwanza ambao umesemwa na wale niliowashukuru; kwanza, ni muhimu sana kufanya sekta ya uvuvi kuwa mamlaka. Kama ambavyo tumefanya kwenye Wakala wa Misitu, tumefanya TANAPA, wote hao wako chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini mamlaka itaongeza chachu ya namna ya kutumia maji yetu ambayo tumepewa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kuongeza pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nashauri, sasa wakati umefika Wizara hii ya Uvuvi pamoja na Mifugo kuwa na vision ya muda mrefu ya nchi. Nilipata faraja sana nilipoona ule mchakato wa Uzinduzi wa Mpango wa Taifa. Nilikuwa disappointed tu kuona kwamba ni miaka 25 peke yake tunawaza, nilifikiri tungewaza miaka 50 ya Mpango wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotupa shida hapa sisi, kwa mfano, tunasema tuna idadi ya ng’ombe milioni 36.6, tuna idadi ya mbuzi milioni 26.6, tuna idadi ya kondoo milioni 9.1, lakini wakati huo huo tumesema tunazalisha maziwa lita bilioni 3.6, maziwa tunayozalisha kwetu. Wakati huo huo tuna idadi ya mifugo wote hao na maziwa yote haya, lakini tumetoa vibali vya watu kuleta maziwa tena hapa nchini kutoka nchi nyingine. Tumetoa vibali 605 vya kuingiza maziwa na lita tulizoingiza ni lita milioni 11.6 za maziwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaweza kuwaza, tuna mifugo hapa mingi sana, tuna lita za maziwa nyingi sana, tunatoa vibali vingine tena 605 vya watu wengine nao walete maziwa hapa. Inawezekana labda hayatoshi kwa maana ya ku-compensate, lakini thamani ya maziwa yaliyoingizwa ilikuwa ni Shilingi bilioni 22.7 thamani ya maziwa ambayo tumeingiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, it doesn’t make sense kama tumetumia fedha ya kigeni kununua maziwa kwa 22.7 billion. Kwa nini tusi-reserve hizi fedha za kigeni, tukaamua kuwa na vision kabisa ya muda mrefu inayohusu uvuvi. Tukasema, uvuvi tuupe vision ya miaka 50 na mifugo tuipe vision ya miaka 50, kuwe na blue print kabisa ya uvuvi na blue print kabisa ya mifugo, ili kila Waziri anapoingia kwenye Wizara hii aikute hii blue print imekaa tayari. Tutajikuta tuna continuation kwenye hizi Wizara na pato litaongezeka. Nachelea sana mtani wangu, kama huna blue print siyo muda mrefu utaanza na wewe kupima samaki pale kwenye restaurant ya Bunge hapo kwa sababu, utakosa cha kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Wizara ya Fedha na Mipango walipoanza kuzindua ule mpango wao wa kuwa na vision ya muda mrefu. Kwa sababu, it doesn’t make sense kwamba tuna TANAPA, ni mamlaka, lakini iko chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii; tuna TFS ni mamlaka iko chini ya Wizara hiyo hiyo; why not uvuvi, tukawa na mamlaka, na hiyo mamlaka ikatengeneza vision ya uvuvi ya muda mrefu, ili kila Waziri anayeingia anatembea kwenye hiyo hiyo vision tukaongeza fedha katika nchi yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia watu wengi sana wanamtia moyo mtani wangu kwamba, pesa aliyopewa ni kidogo. Nikupe siri ya kupata sealing kubwa kwenye hiyo pesa yako. Unless unapeleka vision kubwa kwa mamlaka, mamlaka haiwezi kukupa sealing kubwa. Ukiipelekea mamlaka maono makubwa kwamba, mimi bwana kwenye Wizara yangu, katika eneo la uvuvi nataka kuwa na vision hii hapa. Hii vision italeta asilimia 10 ya pato la Taifa. Hiyo mamlaka itaona hiyo vision yako itakuongezea sealing yako, itakuwa ni rahisi sana, kuliko ile kusema tu kwamba, uongezewe. Za nini? Hata kama ningekuwa ni mimi, nataka kukuongezea mtani wangu, za nini? You don’t lay your plan; you have to lay your plan. It is a proposal that attracts finances. Kwa hiyo, lazima uweke mpango wako wa muda mrefu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nikushukuru wewe binafsi kwa kunipa nafasi ya kuchangia lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo siku kwa siku anaendelea kuongeza bajeti ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nilitishwa sana, wakati Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Magu Mheshimiwa Kiswaga anachangia alisema maneno yafuatayo; nayanukuu alisema kwamba; “Watu wa Jimbo la Magu wamelima mpunga au mahindi na hapo katikati mvua imekatika kwa hiyo, mahindi yamekauka kwa namna yeyote ile watahitaji mahindi ya msaada mwaka ujao kwa sababu watakuwa na njaa” nanukuu alivyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliposikia maneno hayo nilitishika sana na kuogopa sana lile eneo ambalo Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu analitamka liko eneo mita 300 kutoka kwenye Ziwa Victoria narudia tena mita 300 kutokea kwenye Ziwa Victoria mahindi yamekauka na watahitaji chakula cha msaada mwaka ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda niseme mita 300 ni nini? Kiwanja cha mpira kina mita 100. Mita 300 ni viwanja vitatu vya uwanja wa mpira ukiviunga kwa pamoja. Kwa hiyo, wananchi wana mashamba mita 300, mahindi yamekauka, mpunga umekauka, mwaka kesho Serikali itahitaji kuwapa chakula cha msaada au mahindi ya msaada watu wanaoishi kati ya maji yenye uwezo ambayo maji wanaweza wakatumia kwa ajili ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tukubali there is a problem that we must addresses the country lazima tukubali asiyekubali anatatizo binafsi. Sasa basi kwa kusema maneno haya nataka kusema kwamba unless tumefika kwenye agricultural revolution kwa maana ya kuhamisha kilimo chetu na kuingia kwenye kilimo cha umwagiliaji hatutafaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme dunia inakabiliwa na majanga mbalimbali yanayosababisha mabadiliko ya tabianchi na pia mabadiliko ya tabia za wanadamu. Kwa mtu yeyote anayejua projections za dunia, shida ya mvua, mabadiliko ya hali ya hewa yataendelea kuendelea miaka ijayo kwa wingi sana ni kitu gani ambacho kinatuzuia kuwekeza kwa nguvu nyingi sana kwenye suala la umwagiliaji kiasi kwamba tufike wakati tuhame kabisa kwenye kilimo cha kutegemea mvua tutegee umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nani atakaye kuelewa ukisema kwamba mwaka kesho Serikali inategemea kutoa chakula cha msaada kwa watu wanaolima mita 300 kutoka Ziwa Victoria wapate cha msaada? Ni kitu gani hiki kinaendelea? Ni kukosa maono ya muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme watu wanasema hivi kuna namna mbili ambayo kiongozi yeyote tukiwemo Wabunge anatakiwa kuona mambo. Namna ya kwanza a leader must see far more than others kiongozi lazima aone mbali kuliko wengine, a leader must see more than others kiongozi lazima aone zaidi ya wengine, a leader must see before others kiongozi lazima aone kabla ya wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunaona tayari kwamba mwaka kesho tutahitaji chakula cha msaada kwa watu wanaoishi mita 300 kutoka kanda ya Ziwa ya Victoria na wana mashamba pale. Then what do we say? Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo rafiki yangu Bashe ushauri mamlaka tuwekeze sana kwenye kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya vizuri so far so good, so far so good, lakini nilikuwa nakushauri tuwekeze sana, sana kwa sababu mabadilikoo ya hali ya hewa ukiangalia vita duniani mabadiliko ya jiografia, mabadiliko ya kisayansi yanategemewa kuwepo tena na tena. Kwa hiyo, na sisi tuone kwa mbali tuweze ku–invest kwenye umwagiliaji kwa kuwa nchi yetu na Mikoa yetu imezungukwa na maziwa ya kutosha, huo ni ushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili nikuhusiana na Benki ya Mbegu za Asili. Mwaka 1980 watu walianza mchakato wa kuanza Benki ya Dunia ya Mbegu za Asili na kufikia 2008 kule Norway karibu na north pole wakakamilisha kutengeneza benki ya mbegu ya asili ambayo ina mbegu zote za chakula duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata bahati ya kuingia kwenye hiyo benki ya mbegu nikaona literature moja, nilikuwa interested kujua kwanini benki ya mbegu? Literature moja inasema benki ya mbegu kwa sababu watu wana wasiwasi yanaweza kutokea majanga duniani yakaharibu mbegu ama kwa vita ama kwa silaha za nuclear wao ni watakuwa sehemu ya kuuza na kusaidia mbegu duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya pili kwanini benki ya mbegu duniani? Wakasema ni kwa sababu wanahisi kwamba siku zijazo mbegu itakuwa ni biashara kubwa kuliko biashara zote duniani. Hili nalithibitisha kwanza mbegu tulizonazo sasa hivi nyingi ni genetic modified seed zinatoka Ulaya zamani ukipanda yale mazao unayo yavuna unayafanya kuwa mbegu ya mwaka ujao hizi mbegu genetic modified seeds ukipanda yale mazao, ukiyapanda hayawezi yakaota tena inabini ununue na ununue na ununue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utumwa wa mbegu unakuja duniani, narudia tena utumwa wa mbegu unakuja duniani na genetic modified seeds ni nini? Ni mbegu ambazo zimetengenezwa ki–genetic zimewekewa RNA information zina taarifa ndani yake mlaji aweje? Kwa ajili ya nini? Kwa jili ya mambo yajayo waswali wanasema anaekulisha anaamua hatma yako, anaekulisha anaamua utaishi muda gani? Utakuwa na akili gani? Utakuwa na afya kiasi gani? na Taifa lako litakuwaje hapo badae? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri, nashauri sana Wizara ya Kilimo tuweke fedha kwenye taasisi zetu za utafiti tuwe na utafiti wa mbegu zetu za asili na tuwe na benki ya mbegu zetu za asili hapa Tanzania ili ikitokea janga lolote tutatumia mbegu zetu za asili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia hoja hii ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendelea na Makazi.

Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa bidii anazofanya kuzunguka kwenda kila mahali kutupigania sisi Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuchangia hoja hii ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi nataka kuzungumzia kwa habari ya migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali Tanzania, lakini kwa kuwa mimi ni Mbunge wa Jimbo la Kawe nataka tu nijikite zaidi kuzungumza kwa habari ya migogoro ya ardhi katika Wilaya ya Kinondoni. Lazima nikiri kwamba Wilaya ya Kinondoni imekuwa ndio kinara wa migogoro ya ardhi inayochochewa na viongozi wa Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni muhimu sana ku-note hilo jambo kwamba inachochewa na viongozi wa Serikali. Viongozi wa Serikali badala ya ku-solve matatizo ya wananchi kuna baadhi ya viongozi wasio waaminifu wanachochea migogoro ya wananchi na kuwachonganisha na Serikali yao. Nitoe mfano mmoja; kuna kisa kimojawapo ambacho kimetokea kwenye eneo linaitwa Mbweni Mpiji. Mbweni Mpiji siku moja nikapigiwa simu na Katibu wangu (Katibu wa Mbunge) kwamba kuna matrekta, kuna buludoza zinabomoa nyumba za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikakimbia pale Mbweni Mpiji kwenye Kata ya Mbweni jambo la kusikitisha kweli nilikuta nyumba 103 kubwa zimeanguka chini na mbaya zaidi nikakuta baadhi ya watoto wameachwa kwenye hizo nyumba, polisi wanapiga mabomu, kina mama wanachapwa viboko na polisi wamejaa kwenye eneo hilo, sikuamini kwamba hii ndio Tanzania ninayoijua, kilichonishangaza ni kutaka kujua nini sasa kimetokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikamuona OCD kumuuliza je, kuna oda yoyote ya Mahamaka (eviction order) ambayo wewe umekuja kusimamia kubomoa nyumba za wananchi hana, nikawafuata viongozi waliokuwepo pale kama wana hati yoyote hawana, jambo la kushangaza lilikuwa ni hili kwa nini mnabomoa nyumba za wananchi! Wakasema tunabomoa nyumba za wananchi kwa sababu eneo hili kwenye mpango limepangwa kuwa bustani ya miti ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumbuka haijajengwa hiyo bustani, haipo wananchi wamejenga nyumba zao zaidi ya miaka mitano wanaishi, mtu anakwenda kuangusha chini nyumba za wananchi 103 maskini, wananchi walewale ambao mwaka 2020 tumepita tukiwaomba kura za Mheshimiwa Rais na za Mbunge, leo nyumba zao 103 zimeanguka chini wanawake na wanaume wamekamatwa wamepigwa, huyu polisi/OCD anaye-executive hii order hana document yoyote, wanaobomoa hawana document yoyote na hakuna hata mmoja mwenye document. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inashangaza kweli kweli, nikazungumza waliokuwepo Maafisa wa Manispaa, wakasema wameelekezwa na Mkurugenzi wa Halmashauri, nikazungumza na Mkurugenzi wa Halmashauri Dada Hanifa akasema hajawaelekeza, hawana maelekezo yoyote ya kwake, baadaye wakahamia kusema kwamba wamelekezwa na Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa inashangaza kweli viongozi wa kiserikali waliowekwa kwa ajili ya kutetea wananchi, wanakuwa sehemu ya mgogoro ya kuwagombanisha wananchi na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni vizuri kukubali kiongozi yeyote ama wa kisiasa ama wa Serikali inayotokana na Chama cha Mapinduzi jukumu lake la kwanza ni kuhakikisha Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi amekaa kwenye kiti salama na yuko salama katika shughuli zake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, inapotokea kiongozi ama wa kiserikali ama kisiasa anayetokana na Chama cha Mapinduzi hafanyi jukumu hilo basi huyo ni hujuma juu ya Rais wetu na ni hujuma juu ya chama chetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ninapoongea sasa hivi Jimbo la Kawe, lina migogoro ya ardhi mingi hakuna anayeonekana kujali kusuluhisha migogoro hii. Nimefurahishwa sana wiki iliiyopita na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi rafiki yangu Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete, nilizungumza na yeye pamoja na Mheshimiwa Nape wakaja kwenye Jimbo la Kawe kwenye Mtaa wa Jogoo na Ndumbwi, ambao wananchi walikuwa wamezuiwa kuwekewa postcode kwa sababu eneo hilo kwenye mchoro linaonekana eneo la viwanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumbuka ni zaidi 4,500 zimejengwa mle ndani na hakuna kiwanda chochote, hakuna kesi yoyote, hakuna anayewadai, lakini wananchi wamezuiwa kuwekewa postcode kwa sababu linasomeka kwenye ramani ni eneo la viwanda, wameishi miaka 30, Mheshimiwa Nape na Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete wakakaa pale ndani ya masaa mawili, walishatatua mgogoro ulioshindikana kutatuliwa ndani ya miaka 30 iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakwambia Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete pamoja na Mheshimiwa Nape mmefanya kazi nzuri sana na hiyo ndiyo kazi ya kiongozi. Leadership is making decision wether negative or positive, ni afadhali kwa kulaumiwa kwa kufanya maamuzi yasiyo sahihi kuliko kutokuamua kabisa kabisa, nawapongeza sana kwa hiyo kazi mliyofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi viongozi wengi wa kiserikali wasio waaminifu wanachochea migogoro na kumgombanisha Rais pamoja na wapigakura wake. Kwa mfano, kwa dakika chache tu, kule kuna eneo linaitwa Mwembetogwa Boko Chama jana tu wamefika pale wameleta polisi kuwa-harass wananchi, kesi ipo mahakamani lakini wananchi wanakuwa harassed, watu zaidi ya 200 wametolewa kwenye makazi na kesi ipo mahakamani.

Ninaomba sana Wizara ya Ardhi mshughulike sana na suala la migogoro ya wananchi ili tumsaidie Mheshimiwa Rais kuwa na kura zake zilizonona katika Jimbo la Kawe na kuondoa uchonganishi kati ya wananchi na Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru sana kwa kunipa muda ili nichangie na mimi hii hoja ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Kwanza nikushukuru wewe, lakini pia nimshukuru dada yangu Balozi Liberata Lutageruka Mulamula kwa namna alivyo-present hoja yake vizuri kwa ufupi na kwa namna ya kueleweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajikita hasa kwenye suala la uraia pacha; nimeona suala la uraia pacha limeongelewa na watu wengi sana na limekuwa suala la muda mrefu sana. Kwanza nataka nioneshe kwamba uraia pacha duniani siyo issue ngeni, nazitaja kwa ufupi nchi ambazo zinaruhusu uraia pacha; ya kwanza ni Marekani yenyewe, Pakistan, Nigeria, Brazil, Bangladesh, Russia, Mexico, Egypt, Uturuki, Ujerumani, United Kingdom, Ufaransa naweza kuzitaja ni zaidi ya nchi 70 na kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na kuna zingine zimeenda mbali zaidi kama Finland pamoja na Ufaransa wenyewe wameruhusu mpaka multiple maana yake mtu anakuwa na uraia zaidi ya tatu au nne. Sasa siyo issue ngeni duniani kwa sababu zaidi ya nchi 70 na kitu zinakubali suala la uraia pacha. Pamoja na presentation nzuri ya dada yangu Balozi Mulamula, lakini nimekuwa disappointed sana kwa jinsi ambavyo kwenye hotuba yake hakutaja kabisa kwa habari ya uraia pacha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Bunge lililopita tulilizungumza sana kwamba kwa ajili ya kuwasaidia ndugu zetu walio ughaibuni ni muhimu sana ku-consider uraia pacha, lakini kwenye hotuba yake hakuzungumzia kabisa kabisa. Kwa hiyo, nataka nimtangulizie dada yangu Balozi Mulamula nisipopata maelezo mazuri kwenye majumuisho yake ninalo kusudio la kukamata shilingi kwenye mshahara wake, nikipata maelekezo mazuri of course nita-withdraw.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza ambalo nimeona amelikumbuka kwenye hotuba yake ukurasa wa 83 amekubali kwamba kuna remittances kwa maana ya walio ughaibuni diaspora wame-transfer fedha kuja Tanzania mwaka 2020 almost dola milioni 400 na amesema mwaka 2021 wame-transfer fedha dola milioni 569.3; hizi pesa zimetoka ughaibuni au diaspora kuja hapa Tanzania zikiletwa na ndugu zetu walio ughaibuni. (Makofi)

Pia kwenye hotuba yake hiyo hiyo ukurasa wa 83 amesema kwamba hawa ndugu zetu wa diaspora pia wamenunua nyumba National Housing zenye thamani ya bilioni 2.3 na ameongeza pia wame-invest kwenye Hamidu City Park kule Kigamboni. Kwa hiyo, ametambua kabisa mchango wa watu wa diaspora na fedha au remittances ambazo zimetoka ughaibuni kuja hapa Tanzania, lakini namshangaa kwa nini sasa hajaona umuhimu wa kuwaza uraia pacha kwa hawa mabwana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria yetu ya Uraia Sura Na. 357 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002 inatambua uraia wa aina tatu; uraia aina ya kwanza ni uraia wa kuzaliwa, uraia wa kurithi na uraia tajinisi. Sasa uraia wa kurithi ni ule ambao mzazi mmoja ni raia wa Tanzania akizaa mtoto anapewa uraia; uraia tajinisi ni uraia wa kuomba basically mtu anaomba uraia sawa sawa na criteria ya nchi yetu anapewa uraia na uraia wa kuzaliwa ni zawadi ambayo mtu anayoipata kutoka kwa Mungu, hakuna mtu anaweza kuzaliwa nchi mbili kwa mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapozungumza mimi kwa habari ya uraia pacha nilikuwa nakuomba sana Mheshimiwa Mulamula pamoja na wenzako wale Watanzania waliokwenda ughaibuni kutafuta Maisha, mtu amekwenda kusoma, amezaliwa Tannzaia ni Mndendeule, ni Mdigo, ni Mgogo, ni Mpare, ni Mnyaturu akaenda kubangaiza maisha kule na kwenye harakati ya kubangaiza maisha kuna baadhi ya nchi zinauwezo wa kutambua brain za watu wetu, anafanya vizuri Ph.D wanaangalia dissertation yake wanamuona mtu ubongo wake unafaa kutumikia nchi zao, wanawapa uraia, wanabaki kule siyo kwa sababu wanawapenda ili kusudi ile bongo yao itumike kwa ajili ya kuendeleza nchi zao. (Makofi)

Kwa hiyo, sisi kila mwaka na kila wakati tunakuwa tunawapoteza watu hawa kwa kuweka restrictions kwamba hatuwahitaji kuwa raia hawahitaji kuwa raia wa nchi zetu.

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Askofu Gwajima amesema vizuri kuhusu raia wa kurithi, hao raia wa kurithi wakikutana wakaoana huyu raia wa kurithi na huyu raia wa kurithi, wakizaa watoto wanakuwa ni watoto ambao hawana nchi yaani stateless individuals. Kwa hiyo its even worth na naungana mkono na hoja yako.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gwajima.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naipokea hoja ya Mheshimiwa Salome.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hiyo tunakosa mambo ya muhimu sana, kwa mfano Taifa la Israel mwaka 1948 baada ya Wayahudi kuwa wamerudi kutoka kwenye nchi walizokuwa wametawanyika kila Myahudi alirudi na skills za nchi aliyokuwa, matokeo yake Taifa hilo limeendelea sana kiteknolojia kwa sababu kila mtu alikokuwa alirudi na maarifa au skill alizokuwa nazo. Kwa kuwapa watu wetu uraia pacha tunapata faida kadha wa kadha mojawapo ni skill transfer, mtu anakuwa kwenye ile nchi aliyokuwa amekaa ame-acquire skills fulani, anaporudi nchini kama raia wa Tanzania tunaweza ku-tap hiyo skill na kuitumia kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo tunapata tunapata freight capital, kuna baadhi ya Watanzania wamekaa kwenye nchi za kigeni wamefanya vizuri sana kiuchumi. Mimi nilikuwa kule North Caroline nikamkuta Mtanzania mmoja Mnyaturu wa kwetu kule Singida anamiliki University kubwa kama ile University of Dar es Salaam, ni Mtanzania; nilikuwa kule Canada wakati fulani nilikuta Watanzania watatu ni sehemu ya Baraza la Mawaziri katika Serikali ya Canada. (Makofi)

Sasa watu kama hawa tukiruhusu uraia pacha tunaweza ku-tap skills na ku-transfer capital kutoka kwao na tukapata hatua ya nchi yetu kuipeleka mbele zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini faida nyingine kwa kuwanyima uraia pacha tumewatenga na familia zao, ni masikitiko sana unapofika kwenye ubalozi zetu mahala pengine unawakuta wamejipanga kuomba visa ukimsemesha anaongea kindendeule, mwanamke ni Mndendeule, mwanaume ni Mndendeule, watoto Wandendeule wanaomba visa kuja kwenye nchi yao Tanzania, it doesn’t make any sense....

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Gwajima, kengele ya pili hiyo.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie tu kidogo, kwa hiyo kwa sababu hiyo, nilikuwa naomba kama itakupendeza tujitahidi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ni human resource; nchi yetu ina natural resources nyingi sana, lakini natural resources ili uzigeuze ziwe hospitali uzigeuze ziwe shule inahitaji human resource ya watu hawa...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Gwajima mengine unaruhusiwa kuleta kwa maandishi.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja, lakini nisipojibiwa vizuri nitaondoa shilingi, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge kuhusu Wakala wa Kimataifa wa Kimataifa wa Nishati Jadidifu (International Renewable Energy Agency - IRENA) na Azimio la Bunge kuhusu mapendekezo ya kuridhia Mkataba wa Kuanzisha Taasisi ya Dawa ya Afrika wa Mwaka 2019 (Treaty for the Establishment of the African Medicine Agency - AMA)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia katika hoja hii. Kwa makusudi ya kuokoa wakati nitaenda moja kwa moja kwenye Azimio la Bunge kuhusu kuanzisha kwa Taasisi ya Dawa ya Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa maana kwamba tarehe 11 Februari, 2019 ni mahala ambapo Umoja wa Nchi za Kiafrika na wakuu wa nchi walikubaliana kwa pamoja kuanzishwa kwa Taasisi hii ya Dawa ya Afrika. Kwa hiyo nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuwa sehemu ya viongozi hawa na kukubaliana kwenye Mkataba huu wa muhumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, dawa ni matibabu katika ulimwengu wa leo lakini pia dawa ni silaha katika ulimwengu wa leo. Tunapozungumza kuhusu dawa inatoka mahala ambapo si nchini kwetu na inakuja nchini kwetu kwa lengo la kutibu watu ni maeneo muhimu sana kwenye component ya nchi ili tuwalinde watu wetu wawe salama leo, kesho na siku zijazo. Na kwa sababu hiyo nimeona moja ya sababu ya manufaa yanayotokana kuridhia kwa mkataba huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, manufaa ya kwanza ni kuhimarika kwa mfumo wa udhibiti na kuweza kudhibiti bidhaa ambazo haziwezi kudhibitiwa kwa naamna ya kawaida. Wametoa mfano kama bidhaa zinazotokana na genetic au genetic connections. Ninaomba nitoe mfano kwa jambo ambalo nalifahamu vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kuna aina ya matibabu yanaitwa genome editing by Crispr technology. Genome editing by crispr technology ni aina ya matibabu ambayo unamtibu mtu mwenye selimundu (sickle cell) kwa kutumia utalamu wa ku-edit gene yake. Ndugu yangu Daktari Mollel anafaahamu vizuri sana. Matibabu haya ni kwamba una-edit gene ya mtu na unaondoa ule uwepo wa selimundu kwenye genetic inheritance yake ili umtibu. Haya ni matibabu yanayotokana na genetic lakini pia ni matibabu yanaweza kuwa na madhara makubwa kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano kwenye genetic editing by crispr technology ni kwamba utu wa mtu upo kwenye gene ya mtu. Ukifanikiwa ku-edit gene ya mtu unaweza ku-edit utu wa mtu, unaweza ku-edit urefu wake, saizi ya kichwa chake, uwezo wake wa kuelewa, IQ yake, intellectualism yake, rangi ya ngozi na utu wake kwa ujumla.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi Waafrika haatuna maabara za kutosha za kuweza kuchuja kila kitu kinachotoka kwa wenzetu kule magharibi. Sasa kwa Mataifa ya Kiafrika kuja pamoja na kuwa na azimio ya kuanzisha Umoja wa Dawa za Kiafrika inasaidia sana mataifa ya Kiafrika kuwa na maabara ya pamoja kwa ajili ya kudhibiti mambo yenye lengo ya kuiangamiza Afrika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hata kabla sijaenda mbali ninaunga mkono azimio kwa asilimia mia moja pamoja na hayo machache nitakayoyaelezea. Ninaomba ni-highlight jambo moja; katika kila dawa inayotoka nje ya Afrika inaingia kwenye nchi kila nchi inakuwa na jukumu ya ku-analyze hiyo dawa, kujua usalama wake, kujua madhara yake kwa siku za karibuni, siku za kati na siku za mbele. Lakini kama unavyojua kwa mapato ya nchi ya Kiafrika ni nchi za Kiafrika chache sana zenye uwezo wa kufanya jambo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, unakumbuka tulipokaribiwa na chanjo ya COVID-19 tulivyoanza kurukaruka hapa; hakuna Mzungu aliyekuwa tayari kutupa intellectual property ya hiyo chanzo. Lakini tungekuwa tumeishatengeneza tayari Jumuiya ya Kiafrika ya kuziangalia hizi dawa kwa pamoja tungekuwa na maabara za pamoja za Kiafrika zinazochuja dawa zetu zitumikeje na kwamba zina madhara gani kwa siku za karibuni, siku za kati, na siku za usoni. Kwa hiyo azimio hili lazima tuliliridhie kwa haraka na kwa usahihi kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema dawa inatibu lakini pia dawa ni silaha. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jumuhuri ya Muungano ya Tanzania kwa maana hii yeye na wakuu wa nchi wenzake tarehe 11 Februari, 2019 walipoamua kusaini mkataba huu na sisi sasa kama Bunge tunatakiwa kuazimia na kuridhia. Mimi ninalishawishi Bunge lako tuazimie kwa haraka, tuwe na Jumuiya hii ya pamoja, tuwe na maabara za pamoja ili dawa zote zinazotoka nje ya nchi ya Afrika tuwe na uwezo wa kuzichuja na kujua zinawasaidiaje watu wetu; na kama zina madhara iwe ni rahisi kuwa na jukumu la pamoja kama Waafrika kudhibiti na kwenda kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Naomba azimio hili lipite, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa wote wa Mwaka 2022
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia huu Muswada wa Bima ya Afya kwa Watu Wote. Wewe kama Mwalimu wangu wa mambo ya siasa na kiongozi wangu, naomba nikubaliane na maneno uliyoyasema kwamba kwa habari ya Muswada wa Bima ya Afya kwa Watanzania wote, Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi apewe maua yake. Asiyempa maua yake basi ana fitina binafsi, lakini kwa habari ya Muswada huu nasema tena Mama Samia Suluhu Hassan apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikubali kwamba upatikanaji wa dawa nchini umekuwa sana kutoka asilimia 62 mwezi Agosti, 2022 mpaka asilimia 72 mwezi Agosti, 2023. Kwa hiyo, upatikanaji wa dawa umekua sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikubali jambo moja kwamba tumeongeza pia uhaba wa watumishi wa Wizara ya Afya, mpaka sasa hivi tumefikia almost asilimia 50.4, hii ndiyo sababu ninaendelea kusema katika suala hili la afya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan na Waheshimiwa Mawaziri wake wapewe maua yao.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisema jambo moja, asilimia 26.4 ya Watanzania ambao ni kama Watanzania milioni 15.8 wako kwenye umaskini wa kutupwa na hii ni sawa na kaya milioni tatu na laki sita. Hawa wote kwa namna ya kawaida, hawana uwezo kabisa wa kugharamia huduma za afya mahala wanapokaribia kwenda katika vituo vya afya au zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia asilimia nane ya Watanzania ambao ni almost milioni 4 ya watanzania wote ni watu walio kwenye ule umaskini uliokithiri. Almost kaya milioni moja na laki moja ni Watanzania ambao wako kwenye umaskini uliokithiri, hawana uwezo kabisa wa kulipa, kugharamia huduma za afya wao wenyewe. Kwa hiyo, naweza kusema asilimia 85 ya Watanzania hawawezi kupata huduma ya afya inavyotakiwa kwa sababu ya vikwazo vya kifedha walivyonavyo. Naomba ku-declare interest, mimi ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya 2020, Ibara ya 83(e) inazungumza kuisimamia Serikali ili kuwapa Watanzania wote Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hiyo, nataka kuishukuru sana Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan na Waheshimiwa Mawaziri wake, Mheshimiwa Waziri Ummy na Msaidizi wake Mheshimiwa Godwin Mollel kwa kuleta Muswada huu Bungeni ili tuupitishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shakespeare aliwahi kusema; ”mto hauwezi kunywa maji yake wenyewe wala mti hauwezi kukaa chini ya kivuli chake wenyewe.” Ndivyo walivyo Watanzania walio maskini wasioweza kumudu afya, wanahitaji kusemewa na sisi, hawawezi wakajisemea wao wenyewe. Nataka kusema kwa uwazi kabisa hatuwezi kuchelewa hata kwa dakika moja kujadili na kupitisha huu Muswada wa Afya ili Watanzania wote, wanawake kwa wanaume, vijana kwa watoto wapate Bima ya Afya na wao waweze kutibiwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wetu ni maskini sana. Wananchi wetu wengi wanapoteza maisha kwa magonjwa ambayo yanaweza kutibika. Unakuta mtu anaumwa ugonjwa wa kawaida lakini hawezi kumudu matibabu na matokeo yake anapoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ukifungua simu za Waheshimiwa Wabunge, Mbunge yeyote hapa lazima kwenye simu yake utakuta ujumbe au meseji anaambiwa na wapiga kura wa Jimboni kwake nisaidie fedha nikalipe dawa au nisaidie fedha nikalipe hospitali au nina maiti hospitalini nimeshindwa kuitoa kwa sababu za huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu leo bila kufumba macho, bila kupoteza muda tupitishe na tuujadili huu Muswada wa Bima ya Afya ili akina Mama wa Tanzania watibiwe, vijana watibiwe, wazee watibiwe na Watanzania wote kutoka Mashariki, Magharibi, Kaskazini wapate Muswada wa Bima ya Afya na Tanzania iendelee sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimehudhuria misiba minne tofauti iliyobadili mtazamo wangu juu ya Bima ya Afya. Msiba wa kwanza nilihudhuria mahala fulani kule Bunju, nilikuta Balozi mmoja amefariki, Balozi wetu wa Shina, Mwenyekiti wa Shina. Nilipouliza kwa nini alifariki, wanasema alikuwa hana uwezo akaenda kwenye maabara kupima akaonekana ana malaria, lakini akakosa shilingi elfu tatu ya kununua dawa ya malaria. Alikuwa ana shilingi elfu moja ya kupima kuona ana malaria, hakuwa na shilingi elfu tatu ya kununua dawa ya malaria, akarudi nyumbani. Akakaa baada ya muda akazidiwa akapoteza maisha yake. Ni watu wengi wa namna hii nchi yetu ya Tanzania kutoka mashariki mwa Tanzania mpaka magharibi mwa Tanzania, kusini mpaka kaskazini, wanaopoteza maisha kwa magonjwa ambayo yanaweza yakatibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni saa ya wakati wetu, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tupitishe Muswada wa Bima kwa Watanzania Wote, ndugu zetu watibiwe na Tanzania yetu isonge mbele. Falsafa ya bima ni watu wachache wenye uwezo wa kulipa bima walipe bima na hao wachache wanaolipa bima wawafanye watu wengi wasio na uwezo wa kulipa bima wapate faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, inapotokea wagonjwa wote wanakwenda kukata bima, hiyo siyo bima tena. Ninawaomba Watanzania wenye uwezo wa kulipa bima tulipe bima kwa uaminifu kwa ajili ya ndugu zetu wengine ambao wao hawana uwezo wa kulipa bima ili tuwabebe na kwa pamoja mfuko wetu uwe imara na tusonge mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri nilionao, kwa sababu kuna baadhi ya vijiji havina zahanati kabisa, ukienda kule vijijini kuna baadhi ya vijiji havina zahanati kabisa. Hao wananchi na wenyewe ili waweze kutibiwa watalazimika kulipa Bima ya Taifa, Bima ya Afya wakati huohuo hawana mahala pa kutibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali sana ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Waheshimiwa Mawaziri wake, wajitahidi sana maeneo ya vijiji ambavyo hakuna zahanati, wapeleke zahanati ili ile maana ya hawa wananchi na wao kulipa bima walipe bima na wapate mahala pa kutibiwa kuliko walipe bima halafu hawana mahala pa kutibiwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Rwanda ni nchi ndogo sana, hawana rasilimali kama zetu, hawana madini kama yetu lakini wana Bima ya Afya. Hawana milima kama yetu lakini wana Bima ya Afya, hawana mito kama yetu lakini wana Bima ya Afya kwa watu wao. Hawana maziwa kama yetu lakini wanatibu watu wao, hawana bahari kama yetu lakini wanatibu watu wao. Hawana watu wengi kama sisi lakini wanatibu watu wao, hawana ardhi kama ya kwetu lakini wanatibu watu wao, hawana dhahabu, almasi na madini kama ya kwetu lakini wanatibu watu wao. Sisi sasa ni wakati muafaka wa Taifa letu la Tanzania tuwatibu watu wetu wawe na afya njema na naam! Tanzania mpya inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuupitishe Muswada huu wa Sheria ya Bima ya Taifa kwa Watu Wote kwa kishindo na nguvu ili ndugu zetu wote watibiwe. Nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Taifa 2024/2025 ulioletwa mbele yetu na Wizara ya Uwekezaji na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni muumini wa mipango. Tangu niingie katika Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimeongea sana kwa habari ya mipango ya muda mrefu kama njia pekee ya kulipeleka Taifa mahali ambapo linapotakiwa kuwa. Naomba kuzungumza mambo machache ambayo hasa yamekaa kiushauri hasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, ili useme mipango mahali popote katika nchi, data ya kwanza au takwimu ya kwanza ya muhimu ni takwimu ya population. Takwimu ya idadi ya watu ndiyo inaongoza mipango yoyote katika nchi. Idadi ya watu, siyo tu kujua idadi ya watu, ni kuwa na uwezo wa kufanya simulation kwamba kufikia 2050 kwa tunavyoongezeka kwa kuzaana sasa hivi, tutakuwa watu wangapi? Kutokea kwenye simulation hiyo, ndiyo tuweze kupanga mipango ya tunakoelekea baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongee hasa kwa habari ya muundo (structure) wa hii Wizara ya Uwekezaji na Mipango. Nafikiri hii Wizara ni ya muhimu sasa kuliko Wizara zote kwa maana hii; kwenye utangulizi wao wameongea kwa habari ya maandlizi ya dira mpya ya Taifa ya 2050. Ina maana tunataka kutengeneza vision au maono ya nchi ya kufikia 2050, lakini ili watengeneze maono haya kwanza kama nilivyosema ni lazima wafanye simulation. Wawe na uwezo wa ku-imagine, for the rate of population, idadi ya watu inavyoongezeka wawe na uwezo wa ku-foresee au kufanya simulation 2050 Tanzania itakuwa imefikia idadi ya watu wangapi ili vision wanayoiweka kwa ajili ya nchi waiweke kwa kuangalia idadi ya watu itakuwa imefikia kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, pia wawe na uwezo wa kufanya simulation ya technology. Maisha tuliyonayo leo ni tofauti na maisha tutakayokuwa nayo 2050. Technology iliyopo leo, ni tofauti kabisa na teknolojia itakayokuwepo 2050. Kwa hiyo, wanapopanga mipango, ni lazima wawe na uwezo wa ku-foresee kwamba ile vision ya 2050 tunayotaka kuiweka katika nchi ita-match na kiwango cha teknolojia na maisha watakayokuwanayo wakati ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nigusie kidogo tu kuhusu artificial intelligence au ufahamu bandia. Mwaka jana 2022 nilikuwa Uholanzi. Kule kuna gari zisizo na dereva, kuna ma-lawyer robot lakini ni lawyer. Nilikuwa Japan, ma-waiters wengi kwenye hoteli wanawekwa kuwa robot, marubani sasa hivi kwa sababu ya kuepuka ajali, wanaweka robot, wanasheria wanaweka robot, walimu wanaweka robot. Sasa kwenye kupanga mipango ya Taifa, nasi tuweze ku-foresee kwamba tunapopanga mipango ya Taifa tuweze kuona ulimwengu huo tunaouendea wa artificial intelligence (robot): Je, kwa mipango hii tunayopanga leo, itatosha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nikafikiri muundo wa Wizara hii ya Mipango, unatakiwa kuwa tofauti kabisa na muundo wa Wizara nyingine. Kwa mfano, ndugu yangu Kunambi amezungumza hapa akasema kwamba, watu wa madini wamekuja na mpango wao wa 2030, wameutoa wapi? Kwa mfano, ili Wizara ya Mipango ipate mipango yake haitakiwi mtu mmoja au watu wawili au watatu au wataalam wa Wizara hiyo kujifungia ndani na kuanza kupanga mipango ya Taifa ya miaka 2050 ijayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa kufanyika, Wizara ya Maliasili na Utalii na Wataalam wake inaandaa mpango wake wa miaka 50; Wizara ya Ardhi Nyumba na Makazi, inaandaa mpango wake wa miaka 50; Wizara ya Kilimo inaandaa mpango wake wa miaka 50; Wizara ya Maji, Wizara ya Mifugo na Wizara ya Uchukuzi wanaandaa mipango yao ya miaka 50 na Mipango hiyo inapelekwa kwenye Wizara ya Mipango. Halafu Wizara ya Mipango inakuwa inagema kwenye hiyo mipango, inatupa mpango wa mwaka mmoja kama mpango iliyoleta, ili kwamba siku zijazo nchi nzima tuwe na mipango inayofanana na mipango isigongane. Leo tunayoita mipango, siyo mipango bali ni mtiririko wa matukio yanayotokea kwa mpangilio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano kwamba mimi niko Wizara ya Ardhi Maliasili na Utalii. Tunahangaika na Wanyama, wanatoka nje ya hifadhi kwa sababu wanasema maeneo mengi ambayo wanyama wanapita, shoroba zimejengwa. Kwa sababu hiyo, shida ya wanyama kutoka nje ya hifadhi inakuwa kubwa sana kwa sababu shoroba zimejengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shoroba zimejengwa na nani? Ukienda Mvomero pale, Halmashauri ya Mvomero imejenga kwenye ushoroba. UDOM hapo imejengwa kwenye ushoroba, KIA Airport imejengwa kwenye ushoroba na hizi ni taasisi za Serikali zilijenga kwenye ushoroba zikiwa ziomepata building permit. Hii ni kwa sababu ya kukosa maono ya pamoja, kwa hiyo, kama tukipanga maono ya pamoja, tutaondoa contradiction kati ya Wizara hii na Wizara ile na tutaifanya nchi ianze kwenda kwa pamoja kama nchi moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni vizuri sana Wizara ya Ardhi inapeleka maono yake ya miaka 50 Mipango, Wizara ya Fedha inapeleka maono yake ya miaka 50 Mipango, Wizara ya kilimo pia. Halafu Wizara ya Mipango inatoka na vision ya miaka 50 ya nchi yote, inakaribisha na stakeholders wengine ambao ni wataalam wa mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nadikiri kuwa Wizara ya Mipango inatakiwa kuwa na muundo wa tofauti kabisa na Wizara nyingine ili iweze ku-accommodate maono na vision ya nchi kwa pamoja ili tuweze kwenda tunakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tabu ya nchi yetu ni kila mtu ana speed kwa mwelekeo tofauti. Narudia tena, tabu ya nchi yetu ni kila mtu ana speed kwa mwelekeo tofauti. Shakespeare aliwahi kusema, una-speed kubwa sawa sawa lakini je, mwelekeo wako ni sawa? Una Speed kubwa lakini una uhakika wa kufika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shida yetu ni hiyo kwamba, tuna speed kali sana lakini kila mtu kwa mwelekeo tofauti. Kwa mfano, ukiangalia Ripoti ya CAG ina leakage kubwa sana ya fedha za Serikali ambazo kama zingelindwa ingekuwa ni rahisi sana kwenda kule ambako tunataka kwenda sawa sawa na ambavyo tumepanga kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nidokeze kidogo halafu nimalize…

MWENYEKITI: Dakika moja malizia, kengele ya pili imekwishagonga.

MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna idadi ya Wizara 26, kila wizara ikipeleka mipango yake kwenye Wizara ya Mipango, tutakuwa na mipango 26 ya mpaka 2050 iliyoletwa kwa pamoja na hiyo ndiyo itazaa mpango mmoja mmoja wa mwaka ili tuelekee tunakokwenda. Nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru wewe binafsi kwa kunipa muda huu wa kuchangia. Kwa makusudi ya kuokoa muda, nataka nikimbie haraka haraka.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassa, nashukuru Kamati zote za Bunge ambazo zimechakata Miswada hii na kutufikisha mahali hapa tulipofika.

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi sana napenda kuchangia Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango 2023. Nimefurahi sana kwamba Muswada huu au sheria hii itakapotungwa itaipa Tume hii majukumu 19, lakini siwezi kuondoka kabisa bila kugusa Muswada wa Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, niseme machache tu kwenye huo Muswada wa Sheria ya Usalama wa Taifa. Nchi imara yoyote duniani inaanza na shirika la kijasusi imara. Mojawapo ya kazi ya idara ya usalama ni kukusanya taarifa, kuchakata taarifa na kuzipeleka kwa walaji ili walaji wa taarifa waamue kwa wakati na waamue kwa usahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mlaji mkuu wa taarifa Idara ya Usalama wa Taifa ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tulichelewa sana kuihamisha idara hii na kuileta kwenye Ofisi ya Rais, mahali ambapo mlaji mkuu wa taarifa apate taarifa za moja kwa moja. Kwa hiyo, sheria hii inarahisisha sana kazi ya watu wa Idara ya Usalama wa Taifa kumkabidhi mlaji mkuu wa taarifa hizi kwa haraka na kwa usahihi. Ahsante sana kwa Kamati yako kuleta huo Muswada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jambo la pili, ambalo nafikiri ni la muhimu sana, katika kukusanya taarifa popote pale na kuzichakata kuna hatari. Kuna mtu mmoja alisema, kanuni ya kukusanya taarifa ni kwamba lazima taarifa ipatikane kwa ubaya au uzuri, asubuhi au jioni, mchana au usiku, kwenye harusi au msibani. Katika kukusanya taarifa, wakusanya taarifa hawa wanaweza kukutana na shuruba mbalimbali. Kwa hiyo, vifungu vyote ambavyo Kamati ya Bunge imependekeza katika kujaribu kuwalinda hawa wakusanya taarifa, ninazi-support asilimia 100, na zilichelewa tu kuja kwenye Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vile vile, pia sheria hii imechelewa sana. Nashukuru sana Kamati ya Bunge kwa kufanya haya mapema.

Mheshimiwa Spika, niongee kwa uchache sana kwa habari ya Tume ya Mipango ya Taifa na huu Muswada wa Tume ya Mipango ya Taifa. Tangu niingie kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kila nilipopata nafasi ya aina yoyote, nilizungumza kwa habari ya Tume ya Mipango ya Taifa. Nini maana ya mipango ya Taifa? Mipango ya Taifa maana yake ni mwelekeo wa Taifa, ni agenda ya Taifa, ni Dira ya Taifa na ni kesho ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mimi Mhubiri wa Injili, ninukuu Kitabu cha Hosea Sura 4:6 kinachosema “pasipo maono watu huangamia.” Isaya 5:13 inasema, “My people have gone to captivity because of lack of vision.” Yaani, utumwa unakuja kwa kukosa mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi zote za kiafrika ziko kama zilivyo kwa sababu zilikuwa hazijafika mahali zikaichukua hii agenda ya maono ya muda mrefu kuwa priority katika Taifa. Namshukuru Mheshimiwa Rais chini ya Mawaziri wake ambao wameamua kulitengeneza Taifa kwa kuipa agenda ya muda mrefu. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wasiwasi wangu ni ulinzi wa Mipango ya Tume hii. Tutafanyaje ili tume hii na mipango iliyopangwa iwe implemented na kila regime itakayoingia madarakani? Hiyo ni changamoto na ni lazima tuiangalie sana. Kwa mfano, chaguzi zinapoanza kila chama kinaandaa ilani ya uchaguzi. Nashauri ilani ya uchaguzi wa chama chochote ni muhimu i-comply na mpango wa Taifa wa muda mrefu. Maana yake, ilani ya uchaguzi kabla haijaanza kunadiwa (Ilani ya Uchaguzi ni Mkataba kati ya wananchi na chama husika). Chama hicho kikichukua madaraka, ilani hiyo ndiyo inakuwa mpango unaotekelezwa ndani ya miaka mitano ya uhai wa Serikali hiyo. Ni muhimu sana kila chama kinapoanza mchakato wake wa kutengeneza ilani, ilani zake zikaguliwe kwanza na Tume ya Mipango ya Taifa ili chama hicho kikiingia madarakani, kiweze kutekeleza Mpango wa Taifa kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitaka niongee ni ushauri kwamba tusifanye mipango ya miaka 15 au 20, tufanye mipango ya miaka 50 na kuendelea. Mipango hii inaweza kuwa reviewed kulingana na dunia inavyobadilika na uhitaji wa nchi unavyobadilika. Tuwe na mipango ya miaka 50, miaka 100 na kuendelea. Katika kutimiza azma hii ya mipango, tuepuke sana kuwa na msururu wa matukio yanayotokea kwa mwendelezo, tukafikiri hiyo ndiyo mipango.

Mheshimiwa Spika, mipango ni nini? Mipango ni lazima tuwe na kundi la watu wa Tanzania wenye kuiona kesho inapoelekea, wawe na uwezo wa ku-forecast miaka 50 ijayo ya dunia na watafute mipango itakayo-position nchi yetu mahali salama ili iweze kupanda kwenda juu.

Mheshimiwa Spika, kwanza, kwenye hii Tume ya Mipango kuwe na kitengo cha kufanya analysis ya mambo yanayotokea duniani kiuchumi, ki-medicine, kijeshi ili hii idara itakayokuwa kama analysis brain ya hii mipango iweze ku-analyze future. Kwa mfano, tunaona kuna vita kati ya Ukraine na Moscow, Tume hii inatakiwa ku-foresee, vita hii itazaa nini baadaye na Taifa letu litakuwa kwenye position gani baada ya vita hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tuna hzi nchi za China, Moscow, India, Brazil, South Africa ambao wanatafuta kutengeneza currency yao, na wako mwishoni. Dunia inakokwenda, hatutatumia swift kupitia New York, inawezekana kuna namna nyingine ya ku-transfer fedha duniani, ikabadilika. Tume ya Mipango lazima iwe na brain ya ku-foresee dunia mpya itakapozaliwa, mahala ambapo swift haiendi New York tena, Tanzania itakuwaje? So, hii ni vision ya nchi, mipango ya nchi na mwelekeo wa nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tunaweza kusema kwa ufupi, ndani ya miaka 30 nchi yetu kila wilaya iwe na hospitali ya rufaa, ndani ya miaka 30 nchi yetu kila wilaya iwe na university, ndani ya miaka 30 nchi yetu pasiwe na nyumba ya Mtanzania ya majani au ya matembe kama ndugu zangu Wagogo, ndani ya miaka 30 kila nyumba ya Mtanzania iwe na maji safi na salama. Sasa kila regime inapokuja madarakani, inafanya bidii kutimiza mpango huu. Regime yoyote itakayoshindwa kutimiza mipango tuliyojiwekea kama Taifa, regime hiyo itakuwa imeshindwa kuiendeleza nchi sawa sawa na mipango ya nchi. Kwa muktadha huo, hatuhitaji Rais mwenye maono, tunahitaji nchi yenye maono ili Rais atakayeingia afuate maono yetu tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunakuwa na worry sana kwa sababu demokrasia ni namna ya wengi kupata utawala. Kuna wakati demokrasia huwa zina-manufacture watu tusiowategemea. Mussolini alishinda kwenye uchaguzi, Hitler alishinda kwenye uchaguzi lakini kulikuwa hakuna tools au maono ya kuwaongoza kubaki katika mpango wa Ujerumani, wakaingiza dunia kwenye matatizo. Nasi lazima tuwe na break, tuwe na governing machinery ya kuiongoza Tanzania kupitia Tume ya Mipango ambayo ni maono ya nchi, uelekeo wa nchi na hapa naiona Tanzania mpya inakuja kama tutaweza kuishika hii mipango na kuifuata. Naam, Tanzania mpya inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru wewe binafsi kwa kunipa muda huu wa kuchangia. Kwa makusudi ya kuokoa muda, nataka nikimbie haraka haraka.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassa, nashukuru Kamati zote za Bunge ambazo zimechakata Miswada hii na kutufikisha mahali hapa tulipofika.

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi sana napenda kuchangia Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango 2023. Nimefurahi sana kwamba Muswada huu au sheria hii itakapotungwa itaipa Tume hii majukumu 19, lakini siwezi kuondoka kabisa bila kugusa Muswada wa Sheria ya Idara ya Usalama wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, niseme machache tu kwenye huo Muswada wa Sheria ya Usalama wa Taifa. Nchi imara yoyote duniani inaanza na shirika la kijasusi imara. Mojawapo ya kazi ya idara ya usalama ni kukusanya taarifa, kuchakata taarifa na kuzipeleka kwa walaji ili walaji wa taarifa waamue kwa wakati na waamue kwa usahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mlaji mkuu wa taarifa Idara ya Usalama wa Taifa ni Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tulichelewa sana kuihamisha idara hii na kuileta kwenye Ofisi ya Rais, mahali ambapo mlaji mkuu wa taarifa apate taarifa za moja kwa moja. Kwa hiyo, sheria hii inarahisisha sana kazi ya watu wa Idara ya Usalama wa Taifa kumkabidhi mlaji mkuu wa taarifa hizi kwa haraka na kwa usahihi. Ahsante sana kwa Kamati yako kuleta huo Muswada. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Jambo la pili, ambalo nafikiri ni la muhimu sana, katika kukusanya taarifa popote pale na kuzichakata kuna hatari. Kuna mtu mmoja alisema, kanuni ya kukusanya taarifa ni kwamba lazima taarifa ipatikane kwa ubaya au uzuri, asubuhi au jioni, mchana au usiku, kwenye harusi au msibani. Katika kukusanya taarifa, wakusanya taarifa hawa wanaweza kukutana na shuruba mbalimbali. Kwa hiyo, vifungu vyote ambavyo Kamati ya Bunge imependekeza katika kujaribu kuwalinda hawa wakusanya taarifa, ninazi-support asilimia 100, na zilichelewa tu kuja kwenye Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Vile vile, pia sheria hii imechelewa sana. Nashukuru sana Kamati ya Bunge kwa kufanya haya mapema.

Mheshimiwa Spika, niongee kwa uchache sana kwa habari ya Tume ya Mipango ya Taifa na huu Muswada wa Tume ya Mipango ya Taifa. Tangu niingie kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kila nilipopata nafasi ya aina yoyote, nilizungumza kwa habari ya Tume ya Mipango ya Taifa. Nini maana ya mipango ya Taifa? Mipango ya Taifa maana yake ni mwelekeo wa Taifa, ni agenda ya Taifa, ni Dira ya Taifa na ni kesho ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mimi Mhubiri wa Injili, ninukuu Kitabu cha Hosea Sura 4:6 kinachosema “pasipo maono watu huangamia.” Isaya 5:13 inasema, “My people have gone to captivity because of lack of vision.” Yaani, utumwa unakuja kwa kukosa mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi zote za kiafrika ziko kama zilivyo kwa sababu zilikuwa hazijafika mahali zikaichukua hii agenda ya maono ya muda mrefu kuwa priority katika Taifa. Namshukuru Mheshimiwa Rais chini ya Mawaziri wake ambao wameamua kulitengeneza Taifa kwa kuipa agenda ya muda mrefu. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wasiwasi wangu ni ulinzi wa Mipango ya Tume hii. Tutafanyaje ili tume hii na mipango iliyopangwa iwe implemented na kila regime itakayoingia madarakani? Hiyo ni changamoto na ni lazima tuiangalie sana. Kwa mfano, chaguzi zinapoanza kila chama kinaandaa ilani ya uchaguzi. Nashauri ilani ya uchaguzi wa chama chochote ni muhimu i-comply na mpango wa Taifa wa muda mrefu. Maana yake, ilani ya uchaguzi kabla haijaanza kunadiwa (Ilani ya Uchaguzi ni Mkataba kati ya wananchi na chama husika). Chama hicho kikichukua madaraka, ilani hiyo ndiyo inakuwa mpango unaotekelezwa ndani ya miaka mitano ya uhai wa Serikali hiyo. Ni muhimu sana kila chama kinapoanza mchakato wake wa kutengeneza ilani, ilani zake zikaguliwe kwanza na Tume ya Mipango ya Taifa ili chama hicho kikiingia madarakani, kiweze kutekeleza Mpango wa Taifa kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo nilitaka niongee ni ushauri kwamba tusifanye mipango ya miaka 15 au 20, tufanye mipango ya miaka 50 na kuendelea. Mipango hii inaweza kuwa reviewed kulingana na dunia inavyobadilika na uhitaji wa nchi unavyobadilika. Tuwe na mipango ya miaka 50, miaka 100 na kuendelea. Katika kutimiza azma hii ya mipango, tuepuke sana kuwa na msururu wa matukio yanayotokea kwa mwendelezo, tukafikiri hiyo ndiyo mipango.

Mheshimiwa Spika, mipango ni nini? Mipango ni lazima tuwe na kundi la watu wa Tanzania wenye kuiona kesho inapoelekea, wawe na uwezo wa ku-forecast miaka 50 ijayo ya dunia na watafute mipango itakayo-position nchi yetu mahali salama ili iweze kupanda kwenda juu.

Mheshimiwa Spika, kwanza, kwenye hii Tume ya Mipango kuwe na kitengo cha kufanya analysis ya mambo yanayotokea duniani kiuchumi, ki-medicine, kijeshi ili hii idara itakayokuwa kama analysis brain ya hii mipango iweze ku-analyze future. Kwa mfano, tunaona kuna vita kati ya Ukraine na Moscow, Tume hii inatakiwa ku-foresee, vita hii itazaa nini baadaye na Taifa letu litakuwa kwenye position gani baada ya vita hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tuna hzi nchi za China, Moscow, India, Brazil, South Africa ambao wanatafuta kutengeneza currency yao, na wako mwishoni. Dunia inakokwenda, hatutatumia swift kupitia New York, inawezekana kuna namna nyingine ya ku-transfer fedha duniani, ikabadilika. Tume ya Mipango lazima iwe na brain ya ku-foresee dunia mpya itakapozaliwa, mahala ambapo swift haiendi New York tena, Tanzania itakuwaje? So, hii ni vision ya nchi, mipango ya nchi na mwelekeo wa nchi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, tunaweza kusema kwa ufupi, ndani ya miaka 30 nchi yetu kila wilaya iwe na hospitali ya rufaa, ndani ya miaka 30 nchi yetu kila wilaya iwe na university, ndani ya miaka 30 nchi yetu pasiwe na nyumba ya Mtanzania ya majani au ya matembe kama ndugu zangu Wagogo, ndani ya miaka 30 kila nyumba ya Mtanzania iwe na maji safi na salama. Sasa kila regime inapokuja madarakani, inafanya bidii kutimiza mpango huu. Regime yoyote itakayoshindwa kutimiza mipango tuliyojiwekea kama Taifa, regime hiyo itakuwa imeshindwa kuiendeleza nchi sawa sawa na mipango ya nchi. Kwa muktadha huo, hatuhitaji Rais mwenye maono, tunahitaji nchi yenye maono ili Rais atakayeingia afuate maono yetu tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunakuwa na worry sana kwa sababu demokrasia ni namna ya wengi kupata utawala. Kuna wakati demokrasia huwa zina-manufacture watu tusiowategemea. Mussolini alishinda kwenye uchaguzi, Hitler alishinda kwenye uchaguzi lakini kulikuwa hakuna tools au maono ya kuwaongoza kubaki katika mpango wa Ujerumani, wakaingiza dunia kwenye matatizo. Nasi lazima tuwe na break, tuwe na governing machinery ya kuiongoza Tanzania kupitia Tume ya Mipango ambayo ni maono ya nchi, uelekeo wa nchi na hapa naiona Tanzania mpya inakuja kama tutaweza kuishika hii mipango na kuifuata. Naam, Tanzania mpya inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wa Mwaka 2022
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia huu Muswada wa Bima ya Afya kwa Watu Wote. Wewe kama Mwalimu wangu wa mambo ya siasa na kiongozi wangu, naomba nikubaliane na maneno uliyoyasema kwamba kwa habari ya Muswada wa Bima ya Afya kwa Watanzania wote, Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi apewe maua yake. Asiyempa maua yake basi ana fitina binafsi, lakini kwa habari ya Muswada huu nasema tena Mama Samia Suluhu Hassan apewe maua yake. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikubali kwamba upatikanaji wa dawa nchini umekuwa sana kutoka asilimia 62 mwezi Agosti, 2022 mpaka asilimia 72 mwezi Agosti, 2023. Kwa hiyo, upatikanaji wa dawa umekua sana katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nikubali jambo moja kwamba tumeongeza pia uhaba wa watumishi wa Wizara ya Afya, mpaka sasa hivi tumefikia almost asilimia 50.4, hii ndiyo sababu ninaendelea kusema katika suala hili la afya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan na Waheshimiwa Mawaziri wake wapewe maua yao.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nisema jambo moja, asilimia 26.4 ya Watanzania ambao ni kama Watanzania milioni 15.8 wako kwenye umaskini wa kutupwa na hii ni sawa na kaya milioni tatu na laki sita. Hawa wote kwa namna ya kawaida, hawana uwezo kabisa wa kugharamia huduma za afya mahala wanapokaribia kwenda katika vituo vya afya au zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia asilimia nane ya Watanzania ambao ni almost milioni 4 ya watanzania wote ni watu walio kwenye ule umaskini uliokithiri. Almost kaya milioni moja na laki moja ni Watanzania ambao wako kwenye umaskini uliokithiri, hawana uwezo kabisa wa kulipa, kugharamia huduma za afya wao wenyewe. Kwa hiyo, naweza kusema asilimia 85 ya Watanzania hawawezi kupata huduma ya afya inavyotakiwa kwa sababu ya vikwazo vya kifedha walivyonavyo. Naomba ku-declare interest, mimi ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Chama Cha Mapinduzi, Ilani ya Chama Cha Mapinduzi ya 2020, Ibara ya 83(e) inazungumza kuisimamia Serikali ili kuwapa Watanzania wote Bima ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna hiyo, nataka kuishukuru sana Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan na Waheshimiwa Mawaziri wake, Mheshimiwa Waziri Ummy na Msaidizi wake Mheshimiwa Godwin Mollel kwa kuleta Muswada huu Bungeni ili tuupitishe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Shakespeare aliwahi kusema; ”mto hauwezi kunywa maji yake wenyewe wala mti hauwezi kukaa chini ya kivuli chake wenyewe.” Ndivyo walivyo Watanzania walio maskini wasioweza kumudu afya, wanahitaji kusemewa na sisi, hawawezi wakajisemea wao wenyewe. Nataka kusema kwa uwazi kabisa hatuwezi kuchelewa hata kwa dakika moja kujadili na kupitisha huu Muswada wa Afya ili Watanzania wote, wanawake kwa wanaume, vijana kwa watoto wapate Bima ya Afya na wao waweze kutibiwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wetu ni maskini sana. Wananchi wetu wengi wanapoteza maisha kwa magonjwa ambayo yanaweza kutibika. Unakuta mtu anaumwa ugonjwa wa kawaida lakini hawezi kumudu matibabu na matokeo yake anapoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ukifungua simu za Waheshimiwa Wabunge, Mbunge yeyote hapa lazima kwenye simu yake utakuta ujumbe au meseji anaambiwa na wapiga kura wa Jimboni kwake nisaidie fedha nikalipe dawa au nisaidie fedha nikalipe hospitali au nina maiti hospitalini nimeshindwa kuitoa kwa sababu za huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nawaomba sana Waheshimiwa Wabunge wenzangu leo bila kufumba macho, bila kupoteza muda tupitishe na tuujadili huu Muswada wa Bima ya Afya ili akina Mama wa Tanzania watibiwe, vijana watibiwe, wazee watibiwe na Watanzania wote kutoka Mashariki, Magharibi, Kaskazini wapate Muswada wa Bima ya Afya na Tanzania iendelee sawasawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimehudhuria misiba minne tofauti iliyobadili mtazamo wangu juu ya Bima ya Afya. Msiba wa kwanza nilihudhuria mahala fulani kule Bunju, nilikuta Balozi mmoja amefariki, Balozi wetu wa Shina, Mwenyekiti wa Shina. Nilipouliza kwa nini alifariki, wanasema alikuwa hana uwezo akaenda kwenye maabara kupima akaonekana ana malaria, lakini akakosa shilingi elfu tatu ya kununua dawa ya malaria. Alikuwa ana shilingi elfu moja ya kupima kuona ana malaria, hakuwa na shilingi elfu tatu ya kununua dawa ya malaria, akarudi nyumbani. Akakaa baada ya muda akazidiwa akapoteza maisha yake. Ni watu wengi wa namna hii nchi yetu ya Tanzania kutoka mashariki mwa Tanzania mpaka magharibi mwa Tanzania, kusini mpaka kaskazini, wanaopoteza maisha kwa magonjwa ambayo yanaweza yakatibika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni saa ya wakati wetu, Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tupitishe Muswada wa Bima kwa Watanzania Wote, ndugu zetu watibiwe na Tanzania yetu isonge mbele. Falsafa ya bima ni watu wachache wenye uwezo wa kulipa bima walipe bima na hao wachache wanaolipa bima wawafanye watu wengi wasio na uwezo wa kulipa bima wapate faida.

Mheshimiwa Naibu Spika, inapotokea wagonjwa wote wanakwenda kukata bima, hiyo siyo bima tena. Ninawaomba Watanzania wenye uwezo wa kulipa bima tulipe bima kwa uaminifu kwa ajili ya ndugu zetu wengine ambao wao hawana uwezo wa kulipa bima ili tuwabebe na kwa pamoja mfuko wetu uwe imara na tusonge mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri nilionao, kwa sababu kuna baadhi ya vijiji havina zahanati kabisa, ukienda kule vijijini kuna baadhi ya vijiji havina zahanati kabisa. Hao wananchi na wenyewe ili waweze kutibiwa watalazimika kulipa Bima ya Taifa, Bima ya Afya wakati huohuo hawana mahala pa kutibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali sana ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kupitia Waheshimiwa Mawaziri wake, wajitahidi sana maeneo ya vijiji ambavyo hakuna zahanati, wapeleke zahanati ili ile maana ya hawa wananchi na wao kulipa bima walipe bima na wapate mahala pa kutibiwa kuliko walipe bima halafu hawana mahala pa kutibiwa.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Rwanda ni nchi ndogo sana, hawana rasilimali kama zetu, hawana madini kama yetu lakini wana Bima ya Afya. Hawana milima kama yetu lakini wana Bima ya Afya, hawana mito kama yetu lakini wana Bima ya Afya kwa watu wao. Hawana maziwa kama yetu lakini wanatibu watu wao, hawana bahari kama yetu lakini wanatibu watu wao. Hawana watu wengi kama sisi lakini wanatibu watu wao, hawana ardhi kama ya kwetu lakini wanatibu watu wao, hawana dhahabu, almasi na madini kama ya kwetu lakini wanatibu watu wao. Sisi sasa ni wakati muafaka wa Taifa letu la Tanzania tuwatibu watu wetu wawe na afya njema na naam! Tanzania mpya inakuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, ninaunga mkono hoja na ninawaomba Waheshimiwa Wabunge wenzangu tuupitishe Muswada huu wa Sheria ya Bima ya Taifa kwa Watu Wote kwa kishindo na nguvu ili ndugu zetu wote watibiwe. Nakushukuru kwa kunipa nafasi. (Makofi)