Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya (1006 total)

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Ahadi hii ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami imeahidiwa kwa awamu mbili za Marais wetu, akiwemo Rais Jakaya Mrisho Kikwete, mwaka 2010 alikuja Jimboni kwenye kampeni na akaahidi barabara hiyo kwa ujenzi wa kiwango cha lami. Pia Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli naye alikuja 2015 naye aliahidi hivyo hivyo ujenzi wa barabara hyo kwa kiwango cha lami.

Swali ni lini fedha hizi zitapatikana kwasababu sasa hivi ni miaka 10 tunaahidiwa utafutaji wa hizo fedha, ni lini fedha hizo zitapatikana kwa ajili ya upembuzi yakinifu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili,kwa kuwa barabara hiyo inafungua mikoa mitatu na sasa hivi Wilaya ya Nyang’hwale inakimbia kiuchumi, barabara hayo yanaharibika na vumbi jingi katika Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale, hususan pale Karumwa wananchi wanapata adha kubwa kwa vumbi kwasababu magari ni mengi.Je, ni lini Serikali itakomesha vumbi hilo na kuweza kuwanusuru wananchi wa Jimbo hilo na kuweza kuwanusuru wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale hususan Makao Makuu ya Wilaya ya Nyang’hwale Karumwa kupata maradhi mbalimbali yakiwemo TB?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nassor Mbunge wa Nyang’hwale. Ni kweli barabara hii imeahidiwa na Mheshimiwa kama alivyosema Mheshimiwa wa Awamu ya Nne na Mheshimiwa wa Awamu ya Tano, lakini ni azma ya Serikali na ndiyo mpango wa Serikali kwamba katika Awamu hii ya Tano, kipindi cha pili, barabara zote zinazounganisha mikoa na wilaya lazima zitajengwa kwa kiwango cha lami. Kwahiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaamini katika kipindi hiki Serikali itapata fedha na barabara hii itajengwa. Barabara hii pia hata ukienda kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ipo imeahidiwa,kwahiyo ninahakika Serikali itatekeleza.Kwa maana hiyo tutakapokuwa tumejenga kwa kiwango cha lami maana yake hata lile vumbi linaloonekana Karumwa litakuwa limeondoka ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali moja la nyongeza. Kama alivyojibu Mheshimiwa Waziri, barabara hii ni barabara ya kitaifa yaani National Road na ni barabara inayounganisha Mkoa wa Njombe na Morogoro. Kutoka hapo Ifakara sehemu moja mpakani mwa Njombe na Morogoro, Mto Mfuji kuna kilomita takribani 225 na kwa kuwa barabara hii ni muhimu na ni barabara ya kitaifa, je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara kutoka Ifakara ng’ambo ya mto Lumemo kwenda kupita Mlimba, kwenda Mfuji, Madeke Njombe?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kuna haja ya Mheshimiwa Waziri Mkuu…

NAIBU SPIKA: Hilo ni swali la pili? Au hilo hilo la kwanza?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mkuu aliwahi kufanya ziara Jimbo la Mlimba na katika ziara yake aliahidi ujenzi wa kilomita 60. Je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii walau kwa kilomita hizo 60?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Asenga kwa juhudi ambazo anazifanya katika kufuatilia barabara hii ili kuhakikisha kwamba wananchi wa Kilombero wanafaidika na barabara hii ya lami ambayo wanaifuatilia. Baada ya maneno hayo, nitoe tu jibu la jumla, kwamba katika hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati wa kuzindua Bunge hili la Kumi na Mbili, ukurasa wa 26 na 27, Mheshimiwa Rais ameahidi kwamba barabara zenye urefu kilomita 2500 ambazo zinaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami zitakamilishwa katika kipindi hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ameenda mbali zaidi kwenye hotuba kwamba pia barabara zingine ambazo zitaanza kujengwa zenye urefu wa kilomita 6006 ikiwepo barabara hii pia zitakamilishwa ambazo ni zile ambazo ziko kwenye ilani lakini na ahadi zake mwenyewe. Kwa hiyo, nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba hizi barabara Serikali itazikamilisha kama ilivyoahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JACQEULINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwa niaba ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum Rukwa, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Rukwa ni mkoa wenye vivutio vya utalii, lakini pia Mkoa wa Rukwa unajishughulisha na masuala ya uvuvi katika Ziwa Tanganyika. Mkoa wa Rukwa ni mkoa ambao umeshika nafasi ya tatu kitaifa katika uzalishaji wa mazao ya nafaka. Pamoja na hivyo Serikali bado haijajenga uwanja huo. Swali la kwanza, je, Serikali haioni kama ucheleweshaji wa ujenzi wa uwanja huu unasababisha udumavu wa ukuaji kiuchumi wa Mkoa wa Rukwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wananchi wa Mkoa wa Rukwa wamekaa muda mrefu sana hawajapata uwanja wa ndege; je, ni lini Serikali itaanza kujenga uwanja wa ndege wa Mkoa wa Rukwa ili kuwafanya wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanufaike na matunda mazuri ya Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia kuhakikisha kwamba uwanja huu unajengwa. Katika swali la kwanza la nyongeza ameeleza kwamba kuna vivutio vya utalii tunakubali uvuvi, lakini pia ni kati ya mkoa unaozalisha. Serikali tayari imeshapata fedha, sasa hivi kilichopo tu ni kuanza ujenzi. Kwa hiyo, kwa sababu hiyo Serikali imelitambua hili, hivyo, hakutakuwa na sababu ya kuwa na udumavu kwa sababu tayari uwanja huo utaanza haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, ni lini Serikali itaanza kujenga uwanja huo? Katika jibu langu la msingi nimesema kila kitu kimeshakamilika, ni taratibu tu za mwisho za kibenki ambazo lazima zifanyike ili uwanja huo uanze. Kama mkandarasi tayari ameshapatikana kwa hiyo, tuna hakika ujenzi utaanza mara moja. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kwa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri mwenyewe kwamba barabara hii ina umuhimu na sasa kwa miaka miwili imekuwa ikiwekwa kwenye bajeti na haikujengwa na amesema imetegwa shilingi bilioni 5, je, atuambie ni lini atatangaza tenda ili barabara hii ianze kujengwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa anajua wazi kwamba bilioni 5 haiwezi kujenga barabara na barabara hii iko kwenye Ilani ya uchaguzi mwaka 2015-2020 na 2020-2025 na Mheshimiwa Rais ameahidi kwenye kampeni juzi hapa, je, yupo tayari kuweka fedha kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 ili kumaliza kilomita zingine 20 kufika 70 kufikia eneo la Haydom?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Gregory Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini jana pia aliuliza swali la nyongeza lakini leo pia ameleta swali la msingi, kwa hivyo, natambua jinsi anavyofuatilia barabara hii kwa ajili ya wananchi wa Wilaya ya Mbulu. Nimhakikishie kwamba kwa kuwa tayari fedha za awali zimeshatengwa hizo shilingi bilioni 5, kwa hiyo, taratibu za awali zitaanza ikiwa ni pamoja na kutangaza tenda na kufanya shughuli za awali za kuanza ujenzi wa barabara hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu swali namba 28 kwamba Serikali imeahidi barabara zote ambazo imezitolea ahadi katika Ilani lakini pia ni ahadi za Rais katika kipindi cha miaka hii mitano zitatekelezwa ikiwa ni pamoja na barabara hii ya Karatu – Dongobesh - Haydom ambayo Mheshimiwa Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini anaiulizia. Ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kufanya marekebisho, Naibu Waziri amesema Mbunge wa Mbinga Mjini mimi ni Mbunge wa Mbinga Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri yanayotia moyo. Pia nashukuru katika bajeti inayokuja ametutengea kilometa 5. Hofu yangu ni kwamba ikiwa mpango utakuwa ni wa kilometa tano tano barabara hii tunaweza kuikamilisha kwa muda wa miaka kumi na sita na kidogo. Je, Serikali ipo tayari kuongeza kasi ya ujenzi wa barabara hii ambayo imesubiriwa kwa muda mrefu na wananchi wa Jimbo la Mbinga Vijijini, Jimbo la Nyasa na wananchi wa Mkoa wa jirani wa Njombe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hali ya barabara zinazohudumiwa na TANROADS kwa jimbo la Mbinga Vijijini sasa hivi hazipitiki ama zinapitika kwa shida sana. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuzifanya barabara hizi zipitike msimu mzima?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimuombe radhi sana Mheshimiwa Mbunge kwamba huyu ni Mbunge wa Mbinga Vijijini na si Mbinga Mjini. Kwa hiyo, hata wananchi huko wanajua kwamba Mheshimiwa wao wa Mbinga Vijijini yupo anatetea barabara zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno hayo, sasa nijibu maswali yake mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Mbunge anafahamu mara baada ya kuteuliwa hii barabara ni kati ya barabara ambazo mimi nimebahatika kwenda kuzitembelea, kwa hiyo, ninaifahamu vizuri sana. Hata hivyo, tukubali tu kwamba ni jitihada za Serikali kwamba fedha inapopatikana hata kama ni kiasi kidogo zile barabara ziendelee kutengenezwa. Hata hizi kilometa 5 zilizotengenezwa zimesaidia sana kurahisisha usafirishaji wa makaa ya mawe, kwa hiyo, magari makubwa yanayopita pale hayawezi kukwama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini tutatenga fedha zote, Serikali inafanya jitihada fedha zitakazopatikana naamini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kukamilisha barabara hii. Kwa sasa kadri tunavyopata fedha tutaendelea kutengeneza barabara kwa awamu na ndiyo maana hata hizi kilometa tano zilizotengenezwa zimetoa msaada mkubwa sana. Ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nataka niulize swali la nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambayo inawezekana nikayapokea au nisiyapokee.

Mheshimiwa Spika, Bandari ya Mtwara ambayo tulipokea takribani bilioni 153 kwa ajili ya matengenezo makubwa sana. Lakini cha kushangaza bandari hii kwa nini isitumike kwa meli kubwa ambazo zinaweza zikabeba mizigo? Kwa sasa hivi kuna kampuni moja ya meli ambayo kampuni hii inaitwa Sibatanza hawa watu ndiyo ambao wanaleta meli pale peke yao na kuja kufanya kazi ya uchukuzi.

Swali la pili kwa kuwa tumepoteza rasilimali nguvu kazi za watu takribani wachukuzi 6200 wamepoteza ajira kwenye Bandari ya Mtwara ni lini Naibu Waziri tutaongozana kwenda kuzungumza na wale wachukuzi ili waelewe hatma yao ya kazi zao za kila siku walizokuwa wanazifanya kwenye bandari ya Mtwara? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imewekeza shilingi bilioni si 153 lakini bilioni 157 kuboresha Bandari ya Mtwara kwa kujenga gati na kuwekeza fedha nyingi hizi ni ili kuhakikisha kwamba Bandari ya Mtwara inatumika kwa meli kubwa.

Sasa juhudi zinazofanyika mpaka sasa hivi kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, moja ni kwamba Serikali tayari imeshafanya usanifu kujenga chelezo kwa ajili ya kujenga meli yetu chini ya MSCL ambayo itakuwa na uwezo wa kufanya biashara kati ya bandari ya Mtwara na bandari zingine. Lakini tayari Serikali imeshamshawishi mfanyabiashara Dangote aweze kutumia Bandari ya Mtwara kuleta bidhaa zake lakini pia na kusafirisha bidhaa zake.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ushoroba wa Mtwara kuanzia Mtwara, Tunduru, Songea, Mbinga mpaka Mbambabay barabara hii imekamilika tayari Serikali imeshafanya mazungumzo na upande wa wafanyabiashara wa Malawi kwamba waweze kutumia Bandari hii ya Mtwara, lakini pia mazungumzo yapo na upande wa Msumbiji Kaskazini Magharibi ili waweze kutumia bandari hiyo. Kwa maana hiyo tuna uhakika kwamba bandari hii itaendelea kufanyakazi kama ilivyokuwa imekusudiwa ndiyo maana Serikali imewekeza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuongozana na Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga kwenda Mtwara mimi nasema hili halina shida naomba baada ya hapa tukubaliane lini tunakwenda lakini pia tunampongeza Mheshimiwa Mtenga kwa kuhakikisha kwamba bandari hii inafanyakazi. Ahsante sana. (Makofi)
MHE.ZUBERI M.KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba Serikali imewekeza fedha nyingi kwenye Bandari ya Mtwara, lakini commitment ya Serikali katika matumizi ya bandari ile bado haijaonekana. Mfano leo hii kule kuna kitengo cha mafuta (kuna pump ya mafuta ambayo inatakiwa wananchi wa Kanda ya Kusini wote wachukulie mafuta kwenye bandari ya Mtwara lakini ukienda kwa wafanyabiashara bado wanalalamika kwamba mafuta ya Mtwara yako bei juu kuliko Dar es Salaam, matokeo yake watu wanatoka Songea, wanatoka Lindi, wanatoka Tunduru wanafuata mafuta Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, nini kauli ya Serikali namna bandari hii inaweza kutumika efficiently na sisi watu wa Kanda ya Kusini tukanufaika kwa kuwepo kwa bandari hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nini commitment ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa ya Serikali ni kutengeneza miundombinu na tayari commitment ya Serikali imeonekana kuiboresha Bandari ya Mtwara ili iweze kufanya kazi kama ilivyopangwa na ndiyo maana katika jibu langu la msingi sasa tunatangaza na kuitangaza Bandari ya Mtwara ili iweze kutumika kwa sababu sasa inauwezo wa kupokea meli zote kubwa na tungeshauri wafanyabiashara wote waweze kutumia bandari ya Mtwara na hasa wale wa Ukanda wa Kusini. Ahsante.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na kwa kuwa Serikali imekiri kwamba matumizi ya bandari ya Dar es Salaam yalisababisha uharibifu wa barabara ya kutoka Dar es Salaam kwenda Lindi kwenda Mtwara na hali ya barabara hiyo kwa sasa kwa kweli ni mbaya pamoja na kwamba Mheshimiwa Rais aliagiza ikarabatiwe, lakini hali ni mbaya tunasafiri mpaka masaa saba badala ya masaa manne.

Je, Serikali iko tayari sasa kutenga fedha ya kutosha kuikarabati barabara hii kwa kiwango kinachotakiwa ili turudie hali yetu ya zamani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la msingi ilikuwa ni bandari lakini ilikuwa linahusianisha na uharibifu wa barabara kwa sababu magari mengi yanaendelea kutumika. Naomba tu niseme baada ya hapa kwa sababu halikuwa swali la msingi, nitaomba nionane na Mheshimiwa Nape ili niweze kuona namna ambavyo Serikali imetenga fedha kwa sababu ni utaratibu wa Serikali kutenga fedha kufanya matengenezo kwenye barabara zote na hasa barabara muhimu kama hizo.

Lakini figure kamili sina, ila fedha inatengwa kwa kila barabara kuhakikisha kwamba hiyo barabara inatumika. Ahsante. (Makofi)
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba niishukuru Serikali na Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, lakini pia naomba nimuulize swali kwamba eneo lile ni eneo ambalo lina watu wengi kwa maana kata sita katika ukanda ya maji na wakati mwingine kivuko kilichopo huwa kinasombwa na maji kupelekea wananchi wale wanaathirika kwa muda mrefu zaidi na eneo lile lina vituo viwili vya afya ambavyo vina ambulance mbili.

Kwa hiyo, naomba Serikali ione namna ya kufanya haraka katika kuhakikisha kwamba wananchi wale wa Jimbo la Kigoma Kusini katika maeneo yale ya kata sita wanapata ufumbuzi wa jambo hili. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Nashon kwa kufuatilia jambo hili la barabara hii ya Ilagala. Niseme tu mimi Mkoa wa Kigoma nimefanyakazi na barabara hii naifahamu sana, ni kweli anachosema na ndiyo maana Serikali imeamua kutengeneza hili daraja ili kuondokana na adha hii.

Mheshimiwa Spika, tunavyoongea tayari Serikali iko kwenye hatua ya manunuzi ya kufuata Mhandisi Mshauri ambayo inasimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kusombwa na vivuko ni kweli kwamba kwenye daraja hili huu mto Maragalasi ni mto wenye zaidi ya kilometa 300 kwahiyo inawezekana kivuko hiki kinapata changamoto kwasababu ya magogo ambayo yanasombwa na mito na ndiyo maana usiku kivuko hiki huwa hakifanyikazi ila tu kinafanyakazi kunapotokea emergency.

Kwa hiyo tutaendelea na utaratibu huo huo lakini tutahakikisha kwamba hiyo barabara hilo daraja linakamilika mara mara fedha itakapopatikana. Ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza samahani, kwa kuwa leo ni siku yangu ya kwanza na mara yangu ya kwanza kuongea, napenda niwashukuru ndugu zangu wa Morogoro Kusini Mashariki. Pia nishukuru familia yangu, mama yangu mzazi na marehemu mke wangu popote alipo, Mungu amlaze mahali pema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa majibu ya Serikali na kwa kutambua ufinyu wa bajeti na kuzingatia umuhimu wa barabara hii, je, Serikali iko tayari kushirikiana nami kutafuta mkandarasi wa building and finance? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamisi Shabani Taletale, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nimemuelewa vizuri kwamba Serikali itashirikiana naye kutafuta mkandarasi, utaratibu wa kutafuta wakandarasi ni utaratibu ambao uko kisheria na ni utaratibu ambao unatekelezwa na Serikali kupitia mamlaka husika.

Mheshimiwa Maibu Spika, kwa kuwa tumeahidi katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Mheshimiwa Rais katika hotuba yake barabara anayoizungumzia ameiahidi, hivyo, nimhakikishie tu kwamba itajengwa na kukamilika katika kipindi hiki cha miaka mitano ambayo Ilani hii itakuwa inatekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya wananchi wa Makete naomba kuuliza kuhusu ujenzi wa barabara ambayo ipo kwenye Ilani ya kutoka Chimala – Matamba – Kitulo kilometa 51, ilikuwa ni ahadi ya Waziri Mkuu mstaafu, kwa muda wa miaka 10 hadi sasa haijatekelezwa. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoizungumzia Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete ni kati ya barabara ambazo zimetajwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuanzia ukurasa wa 72 – 76. Pia katika kitabu cha hotuba ya Mheshimiwa Rais ameeleza kwamba katika kipindi cha utekelezaji wa Ilani hii pamoja na ahadi alizozitoa atahakikisha kwamba anajenga na kukamilisha barabara zote ambazo zinaendelea zenye urefu wa kilometa 2,500 lakini pia ataanza ujenzi na kukamilisha barabara zenye urefu wa kilometa 6,006 na barabara hii ya Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete ni kati ya barabara ambazo zimetajwa ama zimetolewa ahadi na mwenyewe Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, nimpe uhakika kwamba barabara hiyo itajengwa na kukamilika.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya Bugeme – Nkwenda – Isingiro mpaka Mrongo yenye urefu wa takribani kilometa 135 ikiunganisha Wilaya ya Kyerwa na Karagwe, lakini Kyerwa na Uganda. Swali, ni lini Serikali itakamilisha, ni lini Serikali itajenga hii barabara kwa kiwango cha lami kwa kuzingatia umuhimu wa hiyo barabara na hasa wakazi…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Anatropia swali lako lilivyoisha nilikuwa nimekata maneno. Kwa hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, majibu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge ambaye ameelezea barabara yenye urefu wa kilometa 135 ambayo ni ya Kyerwa – Karagwe, lakini pia inakwenda Uganda:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika swali la nyongeza Mheshimiwa Rais amesema atakapokuwa anakamilisha barabara zote za kilometa 2,500 na kilometa 6,006 tutakuwa tumeunganisha wilaya zote za Tanzania kwa kiwango cha lami, mikoa yote ya Tanzania kwa kiwango cha lami, lakini pia na barabara kuu zote (trunk roads) ambazo zinaunganisha nchi na nchi kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimpe uhakika Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza kwamba, barabara hiyo ni kati ya barabara ambazo zitatekelezwa. (Makofi)
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, pamoja na TANROADS kujitahidi kukarabati barabara ile, lakini nyakati za masika imekuwa ikikata kabisa mawasiloiano; na kwa kuwa, amekiri kwamba, ni muhimu sana kwa kusafirisha mazao na isitoshe wananchi wale wanaitegemea sana barabara ile kwa huduma mbalimbali za kijamii kupeleka wagonjwa hospitali, lakini bidhaa mbalimbali za matumizi ya kila siku. Je, Serikali haioni kwamba, sasa ipewe kipaumbele ili ujenzi wa barabara ile kwa kiwango cha lami uanze haraka iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mkoa wa Mbeya tuna uwanja mkubwa wa ndege wa kimataifa na Mheshimiwa Rais amenunua ndege kubwa, Dreamliner na barabara ile inapita kandokando mwa lango kuu la Kusini kuingia Hifadhi ya Ruaha (Ruaha National Park), sasa watalii wangepitia lango lile la Kusini kwa urahisi kabisa. Je, Serikali haioni kwamba inakosesha pato la Taifa hasa pesa za kigeni? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwa sababu ya umuhimu wa hiyo barabara ndio maana tayari taratibu za kuanza kujenga kwa kiwango cha lami zimeshaanza na zimeshatengwa tayari bilioni 3.38 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mbarali kwamba, kwenye bajeti zinazofuata nina hakika barabara hii itatengewa fedha zaidi, ili iweze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya umuhimu huu kama alivyosema kwenye swali lake la pili kuhusu uwanja wa ndege nasema ndio maana tayari hii barabara kwa Serikali kutambua umuhimu wake ikiwa ni kupokea wageni kutoka uwanja wa Songwe, lakini na kuwapeleka kwenye mbunga, ndio maana tayari taratibu za Serikali zimeanza za kukamilisha ama kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imefanya kazi nzuri ya kujenga barabara kwenye Jiji la Arusha na hasa ukizingatia kwamba, barabara ya mzunguko ya bypass ambayo imesaidia sana kwa watalii na wananchi wa Jiji la Arusha, lakini bado kuna kipande cha Kata ya Moshono ambacho kinatoka eneo la kona ya Kiseliani kuunganisha barabara ya bypass maarufu kama barabara ya T Packers Osunyai kama kilometa saba. Je, Wizara ya Ujenzi haioni sasa ni wakati sahihi wa kumalizia kipande hiki ili kupunguza msongamano na kuweka mazingira mazuri zaidi ya utalii pamoja na wananchi wa Kata ya Moshono?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye ukurasa wa 77 barabara za bypass kwa ajili ya kupunguza msongamano zimeainishwa zikiwemo Miji ya Dar-Es-Salaam, Mbeya na Arusha ni kati ya miji ambayo zitanufaika na barabara hizi za mizunguko kwa ajili ya kupunguza misongamano. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha kwamba, barabara hii aliyoitaja ni moja ya barabara ambazo zitatekelezwa katika kipindi hiki tutakachoanza bajeti katika kipindi hiki cha miaka mitano. Ahsante. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa niaba ya wananchi wangu wa Jimbo la Mbozi napenda kuuliza swali kuhusu Barabara la Mloo – Kamsamba mpaka Kilimamatundu na kutoka Utambalila mpaka Makao Makuu ya Wilaya ya Momba, Chitete, kilometa 145. Kwa kuwa, upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umeshakamilika; na kwa kuwa nyaraka za tenda ziko tayari.

Je, ni lini barabara hii itatengewa fedha na kutangazwa ili ijengwe kwa kiwango cha lami kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi na kama Ilani yetu ya Chama Cha Mapinduzi inavyoelekeza kwa mwaka 2020 - 2025?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoisema ya Mbozi – Mtambalila mpaka Kamsamba ni barabara ambayo, kama alivyosema imeshafanyiwa usanifu na ni kati ya barabara ambazo zimeahidiwa kwanza kwa bajeti zinazokuja zitajengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mwenisongole kwamba, barabara yake iko kwenye mpango na zitaendelea kujengwa barabara kadiri ya fedha itakavyopatikana katika kipindi hiki cha kuanzia mwaka wa fedha wa 2021/2022 mpaka 2025/2026, asante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza kwa kuwa Barabara ya Rujewa – Madibira inafanana na ile barabara ya Arusha – Simanjiro – Kiteto pamoja na Kongwa kilometa 430 ambayo imeahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2020 - 2025 pamoja na hotuba ya Mheshimiwa Rais. Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimjibu Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jibu langu la msingi na bado natambua kwamba, barabara anayoulizia, kama mwenyewe alivyosema, iko kwenye ilani lakini pia iko kwenye ahadi ya Rais, lakini pia iko kwenye hotuba ya Rais.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara hiyo pia, kadiri Serikali itakavyoendelea kutafuta na kadiri fedha zitakavyopatikana ni kati ya barabara ambazo tunategemea kuzikamilisha ili tuweze kuunganisha wilaya zote, mikoa yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali yetu yenye kutia matumaini lakini bado kwa umuhimu wa barabara hii wananchi wa Jimbo la Nachingwea watapenda kusikia commitment ya Serikali. Kwa kweli, katika hili viongozi wengi wanahukumiwa kutokana na barabara hizi pamoja na mambo mengine. Je, nini commitment ya Serikali juu ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, viko vijiji vya Ikungu, Chiola kuelekea Ruangwa, hapa tayari walifanyiwa tathmini na wenzetu wa TANROADS. Watu wa TANROADS walikuja wakafanya tathmini wakiamini kwamba barabara itapita upande wa kulia baada ya muda wakarudi tena wakafanya tathmini upande wa kushoto. Kwa hiyo, hawa wananchi wamezuiliwa kwenye maeneo yale wasifanye maendelezo. Ni lini Serikali itakwenda kutoa ufafanuzi wa jambo hili, ili wananchi wa maeneo yale waweze kuendelea na shughuli zao? Ahsante sana.

SPIKA: Hiyo ni kwa barabara ya Nachingwea – Ruangwa?

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, ndiyo.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Chinguile, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, commitment ya Serikali ni kwamba tayari fedha ya awali za kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami zimeshatengwa. Pia barabara hii imeahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na pia ni kati ya barabara ambayo Mheshimiwa Rais ameahidi kuijenga kwa kiwango cha lami katika kipindi hiki cha miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ambalo ameuliza kwamba kuna wananchi ambao wameshindwa kuendeleza maeneo yao kwa sababu ya watu wa TANROADS waliokwenda kupima, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Nachingwea kwamba suala hili linaendelea kufanyiwa kazi. Naomba kama kuna changamoto yoyote tofauti ambayo pengine mimi nitakuwa siifahamu basi tuwasiliane naye ili niweze kujua changamoto halisi ni ipi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sambamba na barabara ya Masasi – Nachingwea, barabara hii vilevile ina jina la Lukuledi
– Liwale yenye jumla ya kilometa 175 kwa maana kutoka Masasi mpaka Liwale kilometa 175. Barabara hii tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.

Wanaliwale wanataka kusikia barabara Nachingwea – Liwale lini itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja kama nilivyosema tunatambua ni muhimu na zimeahidiwa kujengwa katika bajeti ambayo tutaanza kuijadili. Kwanza ni barabara ambayo ipo kwenye Mpango wa Miaka Mitano na tunategemea katika bajeti inayoanza itatengewa fedha ili ianze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni adhma ya Serikali kuunganisha miji yote ya mikoa na wilaya kwa barabara za lami; na kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hii kiuchumi kwa wananchi wa Mpwapwa, je, Serikali ipo tayari kuipa kipaumbele maalum barabara hii ili ikamilike mapema?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu na ndiyo maana hata hapa tunapoongea yeye atakuwa ni shahidi kwamba mkandarasi yuko site akiwa anajenga hizo kilometa 5. Naamini katika bajeti ijayo tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuendeleza hiyo barabara.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista Joachim Mhagama kwa namna ambavyo halali usiku na mchana anafuatilia kuona kwamba barabara hii inajengwa ili kuweza kuchochea uchumi wa wananchi wa maeneo husika Mkoa wa Ruvuma na Nchi yetu ya Tanzania kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wetu wa Ruvuma ni mkoa ambao umeshika nafasi ya kwanza mara tano mfululizo kwa uzalishaji wa mazao ya nafaka. Wananchi wa maeneo hayo wanajishughulisha na kilimo, uzalishaji wa makaa ya mawe, soko la mazao la Kimataifa, lakini pia kuna shamba la miwa.

Mheshimiwa Naibu Spika…

NAIBU SPIKA: Naomba uulize swali Mheshimiwa.

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa najenga hoja. Swali la kwanza, je, Serikali haioni kuwa kuchelewesha ujenzi wa barabara hii ni kuendelea kufanya udumavu wa maendeleo kwenye maeneo husika hasa kwa Mkoa wa Ruvuma na Jimbo la Peramiho na kwa nchi yetu kwa ujumla? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nafahamu kwamba Kamati ya Bajeti imetenga fedha shilingi milioni 110 kwa ajili ya kufanya usanifu wa ujenzi wa daraja, daraja ambalo limekwishajengwa, daraja la Mkenda. Je, ni kwa nini Serikali sasa isihamishe fedha hii shilingi milioni 110 ikaanze ujenzi wa barabara mara moja ili kuweza kuchochea uchumi wa maeneo husika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii na kwa kutambua umuhimu wa uzalishaji ambao uko katika Mkoa wa Ruvuma lakini pia na makaa ya mawe; katika jibu langu la msingi tumesema barabara hiyo pia ni muhimu sana kwa ulinzi wa nchi yetu na pia ni moja ya vipaumbele vya nchi kuunganisha nchi na nchi na hii ni trunk road wala sio regional road. Ndiyo maana tayari barabara hii imeanza kutengewa fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kama Mheshimiwa Mbunge amenisikiliza vizuri, kulifanyika usanifu wa awali ambao wakati huo barabara haikuwa na matumizi ambayo inayo sasa hivi na ndiyo maana kukafanyika redesign yaani usanifu mpya kwa sababu tayari sasa kule kuna makaa ya mawe na mgari yaliyokuwa yanapita wakati ule wakati barabara inafanyiwa usanifu siyo ambayo sasa yanapitika. Kwa hiyo lazima lile daraja lifanyiwe usanifu mpya ili liweze kumudu shughuli ambazo sasa zitaweza kufanyika kwa maana ya kuwa na uwezo wa kuhimili magari ambayo yatapita na uzito wake hasa baada ya kugundua makaa ya mawe na kuongezeka kwa traffic kwenye hiyo njia. Ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu, lakini pia swali hilo linafanana na hali ya kule Mufindi. Kwa kuwa Mufindi ni kitovu cha viwanda nchini na zaidi ya viwanda tisa viko pale na miundombinu imekuwa ni mibovu sana; na kwa kuwa barabara ya Nyololo - Mtwango na Mafinga - Mgololo zimeahidiwa kuanzia wakati wa Mwalimu Nyerere, pamoja na Rais Magufuli, zimeahidiwa na Mawaziri Wakuu, Mzee Pinda na Mzee Kassim Majaliwa, zimetajwa kwenye Ilani ya CCM karibu mara tatu…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kuingiza kwenye bajeti barabara hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara zote alizozitaja zinakwenda kwenye maeneo ya uzalishaji mkubwa sana ambao yanachangia fedha nyingi sana kwenye Mfuko wa Serikali na kama alivyosema barabara hizo zimeahidiwa na viongozi wengi wa Kitaifa, lakini pia barabara hizo zimetajwa kwenye Ilani, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizo kwa sababu ya umuhimu wake, kuanzia bajeti inayokuja zitaanza kutengewa fedha ili ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya barabara hiyo kutoka Kijiji cha Misegese kufika Malinyi Mjini huwa haifikiki kipindi chote, hata mvua ikinyesha siku moja tu, tunalazimika kutumia mitumbwi kufika Malinyi Mjini na magari hayafiki kabisa. Mkandarasi ambaye yuko site anaweka calavat moja badala ya yanayotakiwa kama sita au saba. Amepewa kazi ya kuinua tuta mita 200 badala ya kilometa moja ambayo ni uhitaji halisi. Je, Serikali haioni haja ya kumuongezea uwezo kujenga kulingana na uhitaji ambao nimeutaja?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuongozana na mimi kwenda Malinyi baada ya Bunge hili ili kujionea hali halisi ya miundombinu na kutafuta suluhisho la pamoja? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mgungusi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nitaanza na swali la mwisho, naomba niseme kwamba barabara hii imekuwa inaulizwa sana na Waheshimiwa Wabunge wengi ambao ni wanufaika wa barabara hiyo. Kwa hiyo, niwadhihirishie ama niwaaminishe kwamba mara baada ya kikao hiki nitahakikisha naitembelea barabara hiyo ili niweze kuifahamu vizuri kwa sababu kila mara Wabunge wa eneo hilo wananifuata kwa ajili ya kutafuta utatuzi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili alilouliza kuhusiana na tuta linalojengwa na mkandarasi, naomba Mheshimiwa Mbunge Mgungusi kwa sababu, bahati nzuri mkandarasi yuko site, tutaongea na Meneja wa TANROADS ambaye ndiye anamsimamia mkandarasi huyu ili kama kuna shida ya kitaalamu ama ya uwezo, Serikali tutahakikisha kwamba tunampa maelekezo ya afanye vile inavyotakiwa kama ambavyo ipo kwenye design. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mara kwa mara Serikali imekuwa ikizungumzia kujenga barabara inayotoka Mtwara Mjini kuelekea Msimbati ambako kuna mitambo na visima vya gesi. Je, ni lini sasa Serikali itajenga barabara hiyo muhimu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Shamsia kwamba katika kitu ambacho Serikali ya Awamu ya Tano inakifanya, kwanza tumetoa ahadi kujengwa kwa barabara za wilaya, mkoa na za kitaifa na barabara zile ambazo zinaenda maeneo muhimu kwa maana ya uchumi wa Taifa. Kwa hiyo, kama barabara hiyo inaangukia humo, nataka nimhakikishie kwamba kuanzia bajeti tunazoanza na katika Mpango huu ambao tunaendelea nao, nina hakika katika miaka mitano barabara hii itakuwa imejengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kama ilivyo kwa barabara hii ya Lupiro – Malinyi, barabara ya Korogwe – Dindira – Bumbuli mpaka Soni iliahidiwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, lakini pia kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ilikamilika. Napenda kujua, ni lini sasa kazi ya ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami itaanza ili kuwasaidia wananchi wa Korogwe na Lushoto kwenye eneo la usafiri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge ambaye ameuliza barabara ya Korogwe hadi Soni ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Wabunge wawe na imani na Serikali hii ya Awamu ya Tano kwani kwanza ni ahadi za viongozi wetu wa kitaifa Mheshimiwa Rais lakini pia zimetajwa katika Ilani. Naomba tuanze bajeti na nina hakika hizi barabara ambazo tunaziulizia zimo, kwa sababu tumeahidi tutatengeneza hizi barabara kwa kiwango cha lami. Nashauri Waheshimiwa Wabunge wawe na imani kwamba barabara hizi zitajengwa ikiwa ni pamoja na barabara ya Korogwe kwenda Soni. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, ni nini kauli ya Serikali kwa kumalizia kipande cha Mbande – Kisewe ambacho kimekuwa ni kero kubwa kwa wananchi wa Kata ya Chamazi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa, barabara ya Zakhem – Mbagala Kuu imepata fedha za Mradi wa Uboreshaji wa Jiji la Dar-Es-Salaam na imeshindwa kujengwa kwa sababu ya uwepo wa bomba la mafuta la TAZAMA. Je, Serikali ina mpango gani wa kulipa fidia walao corridor ya mita saba ili barabara hiyo ambayo tayari inayo fedha iweze kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi tunavyoongea sasa hivi, Mheshimiwa Chaurembo ni shahidi, tulikuwa na kilometa 6.05; kilometa moja imeshakamilika zimebaki kilometa 5.06. Nimhakikishie Mheshimiwa Chaurembo katika mwaka huu wa bajeti, kupitia fedha ya matengenezo, sasa tutaanza barabara ya kutoka Mbande kuja Msongola ambapo tunajenga kilometa 1.5 kwa kiwango cha lami. Pia kwa fedha ya maendeleo tutaendelea kutoka Msongola kwenda Mbande kilometa 1. Kwa hiyo, tutabakiwa kama na kilometa 2.5 ambazo zitakuwa bado hazijakamilika na fedha itakapopatikana tutaendelea kukamilisha barabara hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la kuhamisha bomba ama barabara Serikali imelipokea na itakwenda kulifanyia kazi tuone kama tutahamisha kwa sababu inapita karibu na bomba. Tutaangalia namna ya kufanya ili barabara ile muhimu sana iweze kuanza kujengwa. Pia kwa sababu suala hili siyo la Idara yangu pekee kwa maana ya Wizara ya Ujenzi ni Wizara nyingi, kwa hiyo, tumelipokea na tutakwenda kulifanyia kazi kuona ni namna gani tufanye kuhamisha barabara hiyo. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Swali la kwanza; barabara hii ni muhimu sana kwa shughuli za uchumi wa wananchi wa Lushoto, hasa ukizingatia kwamba, mazao tunayozalisha kule ni mbogamboga na matunda ambayo ni rahisi kuharibika. Kulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, angalau sasa barabara hii ijengwe japo kwa kiwango cha kilometa 10 kwa mwaka. Je, tunapoelekea kutengeneza bajeti Serikali haioni ni muhimu kutenga kiwango hicho cha kilometa 10 kwa kila mwaka?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa barabara hii imeendelea kutia hasara wananchi wa Mlalo, hasa nyakati za mvua. Je, Serikali sasa iko tayari kuwalipa fidia mara ambapo wananchi wanapata hasara ya mazao yao kuoza barabarani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hii ambako kunazalishwa sana matunda na mbogamboga. Kwa kutambua umuhimu huo ndio maana Serikali tayari imeshakuwa na mpango wa kujenga hii barabara. Tunatambua pia kwamba, Serikali ilitoa ahadi kwamba, itaendela kujenga hii barabara walao kwa kilometa 10.

Mheshimiwa Naibu Spika, ameuliza kama kwenye bajeti ijayo je, tutajenga. Itategemea pia na upatikanaji wa fedha na kama itapatikana si tu kilometa 10 bali inawezekana ikawa ni kukamilisha kabisa barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; endapo kama tutatoa fidia kwa wale wanaopata matatizo hasa pale ambapo mazao yao yanaharibika. Tumeshaongea na Meneja wa TANROADS Mkoa wa Tanga, ili badala ya kuendelea kutengeneza kile kipande wanachokiendeleza, basi atengeneze yale maeneo ambayo ni korofi, ili yaweze kuimarika na kusitokee tatizo kama hilo. Kama kuna changamoto nyingine basi namwomba Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo, anipatie. Nimwahidi Mheshimiwa kwamba, nitafika kuona hizo changamoto ambazo anazisema. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona, nilitaka kunyosha mikono miwili. Naomba niulize swali moja. Kwa vile Mheshimiwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipokuwa kwenye kampeni kule Vunjo aliahidi kujenga barabara ya Kilema a.k.a barabara ya Nyerere ambayo ni kilometa tisa; barabara ya Uchira kwenda Kisomachi kilometa nane tu na Mabogini – Kahe na Chekereni ambayo na yenyewe ni kilometa 22 tu kwa kiwango cha lami. Je, Mheshimiwa Waziri anaweza akatuhakikishia kwamba, barabara hizo zimeingizwa kwenye mpango wa 2021/2022? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi alizosema ni ahadi za Rais na ni ahadi katika kipindi cha uchaguzi wa 2020. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Kimei avute subira kwa sababu, bajeti ndio inaenda kwa hiyo, tutaangalia. Siwezi nikasema kwa sasa kwa sababu, hiyo bajeti bado haijapitishwa, lakini kama ni ahadi ya Rais, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba, ahadi za Rais zitazingatiwa katika kutekelezwa kwa bajeti zinazokuja kuanzia 2021/2022. Ahsante. (Makofi)
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali nataka kufahamu ni hatua gani za kinidhamu zinazoweza kuchukuliwa na Serikali kwa wataalam wetu wanaosababisha variation ya miradi kuwa na gharama kubwa, kwa mfano, daraja hili la Mbaka ambalo limechukua muda mrefu sana. Kuna kitu tunaita geotechnical investigation hakikufanyika na ndiyo maana imechukua muda mrefu zaidi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa daraja hili litakapokamilika kutakuwa kuna madaraja mawili, kutakuwa kuna daraja hili ambalo linajengwa pamoja na lililokuwepo la chuma.

Je, Serikali ipo tayari kulichukua hili daraja la chuma kupeleka katika mto huo huo Mbaka lakini kwa kuweza kuunganisha kati ya Majimbo ya Busokelo, Kyela pamoja na Rungwe katika Kijiji cha Nsanga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari ni utaratibu wa Serikali pale ambapo mfanyakazi yeyote amefanya kinyume na utaratibu anachukuliwa hatua na kwa sababu umakini huo ndiyo maana ilionekana kwamba daraja hili lilikosewa design na ikafanyiwa redesign na tayari ujenzi unaendelea kwa hiyo ni utaratibu wa kawaida pale panapotokea tatizo hatua zinachukuliwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, anauliza endapo daraja la chuma lililokuwepo litakwenda kwenye daraja lingine alilolisema ni utaratibu wa Serikali kwamba madaraja haya ya chuma ni madaraja ambayo yanatumika kwa ajili hasa ya dharura. Kwa hiyo utaratibu utawekwa kama itaonekana ni muhimu liende hapo litakwenda lakini vinginevyo tunayatunza maeneo ambayo ni ya kimkakati ili kunapotokea tatizo la dharura basi hayo madaraja yatakwenda hapo. Ahsante.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa upembuzi yakinifu wa kipande cha Ifakara – Kihansi chenye kilometa 125 umekamilika. Je, Serikali iko tayari kuanza kutenga fedha ya kujenga hiki kipande katika mwaka huu wa fedha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili barabara ya Lutamba- Chiponda-Mnara-Nyengedi inayounganisha Halmashauri ya Mtama na Halmashauri ya Manispaa ya Lindi ambayo pia inaunganisha barabara ya Mkoa ya kwenda Ruangwa lakini pia ya kwenda Masasi kwa maana ya Mkoa wa Mtwara, ni barabara ya muhimu sana kwa uchumi wa eneo hili, lakini hii barabara imekuwa chini ya TARURA kwa muda mrefu na TARURA kwa kweli hawana uwezo wa kuendelea kuijenga. Je, Serikali iko tayari kuipandisha hadhi barabara hii sasa ianze kuhudumiwa na TANROADS?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Nape, Mbunge wa Mtama, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoiuliza ya Mheshimiwa Kunambi ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa na Mkoa na kwa kuwa usanifu wa kina umekamilika, tunaamini katika bajeti ijayo Serikali itaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Nikiri Mheshimiwa Kunambi kila anaposimama imekuwa akiipigia sana kelele barabara hii. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi kwamba katika bajeti tunazoanza kuzitekeleza kwa mwaka ujao naamini itatengewa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili la Mheshimiwa Nape Mbunge wa Mtama sitazitaja barabara zake zimekuwa ni nyingi Lutamba-Chiponda-Mtama-Lindi na kwamba ni barabara za TARURA, naomba Mheshimiwa Nape nimshauri waweze kupitia kwenye taratibu za kawaida za kupandisha hadhi hizi barabara kutoka TARURA kwenda TANROADS ambapo lazima watakaa na Bodi ya Barabara ya Mkoa halafu itakwenda kwenye Kamati ya Ushauri ya Mkoa na baadaye zinakuja kwenye Wizara kwa ajili ya kuziangalia kama zinakwenda kupandishwa hadhi. Kwa hiyo kama zitakuja kwa utaratibu huo nadhani kuna utaratibu zitafikiriwa na Serikali itaona namna gani ifanye ili kuzipandisha hizo hadhi. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwa majibu ya Serikali na nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri na weledi katika masuala yote ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza na swali la kwanza ni barabara ya Katoma - Bukwali ambayo ni barabara inaunganisha nchi yetu nanchi ya Uganda na ni barabara muhimu kwa uchumi kwa wananchi wa kata za Gera, Ishozi, Bwanjai, Kashenye na Kanyigo; barabara hiyo yenye kilometa 39.5 nishukuru Serikali sasa hivi kilometa nne zimeanza kujengwa kwa kiwango cha lami na je ni lini kilometa 35.8 zilizobaki zitawekwa kwenye bajeti na kuweza kukamilishwa kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni barabara ya Bunazi - Nyabiyanga - Kasambya - Kakindo na Minziro ambayo barabara hiyo inaunganisha Makao Makuu ya Wilaya pamoja na nchi yetu ya Uganda lakini kuwa ni barabara kiungo kwa wananchi wote wa Tanzania kila mwezi Januari wananchi wanaenda kuhiji katika eneo takatifu la Mtakatifu Yohana Maria Muzeyi aliyezikwa hapo na ni mojawapo ya mashahidi 22 wa Uganda.

Je, ni lini barabara hiyo yenye kilometa 35.8 na yenyewe itaweza kutengenezwa kwa kiwango cha lami nakushukuru kwa nafasi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika,kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Florent Laurent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ya Katoma - Bukwali tayari ipo inaendelea kujengwa na kilometa
4.2 kama alivyosema zinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana na mimi kwamba bado wakandarasi wawili wako site wakiwa wanaendelea kufanya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami kwa kilomita ambazo tunaamini kilometa 2.2 zitakamilika mwezi Aprili na Serikali bado inaendelea kutafuta fedha na katika bajeti ijayo barabara hii tunaamini kwamba itapata fedha kuendelea kukamilishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara alizozitaja zote hizo za vijiji mbalimbali na kata mbalimbali tunatambua kwamba ni muhimu kwa uchumi wa wananchi wa Nkenge na bado Serikali tunaahidi kwamba itaendelea kuzikarabati na pale fedha itakapopatikana kuzijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa fursa ya kunipa kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ubovu mkubwa wa miundombinu ndani ya Jimbo la Momba. Je, ni lini Serikali itatusaidia kutujengea kilometa 15 za kiwango cha lami kwenye Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Momba katika Kata ya Chitete ikiwa ni sambamba na ahadi ya mama yangu mpendwa Mheshimiwa Makamu wa Rais alipotembelea Jimbo la Momba tarehe 13 Oktoba, 2020 alituahidi angeweza kutusaidia barabara hiyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naombakujibuswali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Momba kama ifuatavyo:-

MheshimiwaNaibu Spika, ni kweli ahadi ya Makamu wa Rais wakati wa kampeni ilitolewa mwaka huu wa kampeni 2020; kwa hiyo, kama Serikali ahadi hii tumeichukua na tunaifanyiakazi. Kwa hiyo, katika awamu inayokuja ya bajeti tunategemea kwamba zitakuwa ni kati ya barabara ambazo zitatengewa fedha na once zikitengewa fedha barabara hiyo itajengwa.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, naomba niulize Serikali na wananchi wa Sikonge wanasikiliza na Mkoa wa Tabora; je, baada ya kuwa Serikali imekamilisha maandalizi yote ya ujenzi wa kiwango cha lami barabara ya Ipole - Lungwa yamekamilika usanifu kila kitu. Je, sasa bado fedha na mkandarasi Serikali itaanza lini kujenga barabara hiyo ili kuunganisha Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Tabora?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Ipole - Lungwa ni kati ya barabara zinazounganisha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Mbeya na kama alivyosema taratibu zote zimekamilika, kinachotegemewa tu ni lini itatangazwa kwa sababu sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya manunuzi kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na kama alivyosema wananchi wake wanamsikia ni barabara muhimu inayounganisha na mkoa na mkoa, kwa hiyo ninahakika barabara hii itatengewa bajeti na taratibu za manunuzi once zikikamilika basi tutakuwa tumepata mkandarasi na itaanza kutekelezwa, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa matatizo yanayowapata wananchi wa Tunduru yanafanana kabisa na matatizo ambayo yanawapata wananchi wa Kigamboni katika Mkoa wa Dar es Salaam. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga barabara ya Kibada - Kisarawe Two - Mwasonga - Tumbi Msongani ili kuwasaidia wananchi Wilaya ya Kigamboni waweze kupata unafuu wa usafiri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam kuhusu barabara za Kigamboni. Hiki ni kipindi cha bajeti na kama tulivyoahidi barabara hizi zitajengwa ndani ya miaka mitano, kwa hiyo kwenye bajeti pengine suala la kuanza usanifu wa awali na wa kina litajitokeza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi kama tulivyoahidi zitajengwa. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ya Mgakolongo kwenda Kigalama mpaka Mlongo inayounganisha na nchi ya Uganda, usanifu wake umeshakamilika muda mrefu. Ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye Ilani na nimuombe Mheshimiwa Mbunge awe na subira tuone bajeti ambayo tunaiandaa hiyo barabara itashughulikiwaje. Kwa sasa siwezi nikasema chochote maana ndiyo tuko kwenye kipindi cha bajeti, kwa hiyo, naomba awe na subira aone kama barabara yake itajengwa lakini tunatambua ni barabara muhimu sana. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Changamoto ya barabara iliyoko Tunduru Kusini inafanana kabisa na changamoto iliyoko wilaya ya Ngara ya barabara ya Murugalama - Lulenge - Mizani yenye urefu wa kilomita 85. Je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu swali la nyongeza la kwanza, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hii barabara aliyoitaja ambayo inapita eneo la Mgalama - Lulenge nina hakika zitajadiliwa katika kipindi hiki cha bajeti, kwa hiyo, awe na subira.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa jibu la Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninatambua jitihada za Serikali kuboresha usafiri kati ya Rugezi kwenda Kisorya. Hata hivyo, kutokamilika kwa hili eneo la Lot III na hasa barabara ile ya kilometa 14 kutoka Rugezi – Nansio inaathiri sana uchumi wa wananchi wa Ukerewe, na ndiyo maana tarehe 04 Septemba, 2021 Hayati Dkt. John Magufuli akiwa Ukerewe, kwa kutambua changamoto hizi alitoa maelekezo eneo hili lifanyiwe kazi mara moja. Mwaka jana Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa Ukerewe alisisitiza jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwanini sasa Wizara isione umuhimu wa jambo hili ikatenga pesa kwa haraka ikaufanya kama mradi wa haraka ili Lot III, hasa wakati wanasubiri pesa za kujenga daraja basi barabara km. 14 kati ya Rugezi kwenda Nansio iweze kukamilika kwa haraka?

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mkundi Mbunge wa ukerewe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Ukerewe. Lakini Mheshimiwa Mbunge yeye pia atatambua kwamba Serikali inafanya jitihda kubwa sana kuhakikisha kwamba inatengeneza barabara na ndiyo maana imegawanywa kwenye Lot III. Lot ya pili imeshakamilika, lot ya kwanza mkandarasi yuko site na Serikali imeahidi kwamba inatafuta fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, daraja tunaloliongelea urefu wake unafanana na daraja karibu lile linalojengwa la pale Surrender Bridge, ni takriban kilometa moja. Kwa hiyo Serikali lazima ihakikishe kwamba inajitahidi kupata fedha ya kutosha ili kuweza kujenga daraja hilo; na ndiyo maana tayari usanifu wa kina umeshafanyika. Tayari Serikali imeonesha jitihada za makusudi, kwamba kwanza ni ahadi ya Hayati Rais, lakini pia Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwa hiyo Serikali kama nilivyosema kwenye jibu la msingi inaendelea kutafuta fedha na fedha ikipatikana nina uhakika kipande hiki cha Lot ya tatu kitajengwa. Ahsante.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa tuko katika Wizara ya Ujenzi, na Wizara hii ndiyo inayoshughulikia barabara pamoja na madaraja, sasa nilitaka kuuliza swali linalohusu barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alitutembelea kule Milola na tukampa kero yetu ya barabara ambayo inatoka Ngongo inapitia Rutamba, Milola hatimaye inamalizikia Ruangwa. Mheshimiwa Waziri Mkuu alituahidi kwamba barabara ile itajengwa kwa kiwango cha lami.

Sasa, je, ni lini barabara ile itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongezala Mheshimiwa Salma Kikwete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu ipo kwenye mipango, na ninaamini usanifu wa awali unaweza ukaanza kwa sababu hatujapita bado kwenye bajeti. Niombe kujiridhisha, Mheshimiwa Salma nimuombe baada ya kikao hiki pengine tuweze kukutana naye ili tuweze kuona barabara hii iko kwenye mpango kwasababu sasa hivi tuko bajeti kwa hiyo ni ngumu kusema barabara hii iko kwenye hatua gani. Kama ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu na kama iko kwenye ilani naamini itakuwa ni barabara ambazo ziko kwenye matazimio ya kufanyiwa kazi na hasa upembuzi yakinifu. Ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuwa barabara inayoanzia King’ori, hadi Ngarenanyuki imekuwa kero kubwa sana kwa wananchi wa Jimbo la Arumeru Mashariki, na Serikali imekuwa ikiahidi mara nyingi kujenga barabara ii katika kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka kufahamu ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi yake kwa wananchi wa Arumeru Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Magige kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba ni lini barabara ya Kilole kwenda Ngarenanyuki itajengwa kwa kiwango cha lami. Barabara hizi zote ambazo zimeainishwa tuna uhakika tutazikamilisha katika kipindi hiki cha miaka mitano. Lazima kutakuwa na mahali tutaanza na barabara chache lakini tutamaliza zote. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara zote ambazo zimeainishwa na ambazo zimeahidiwa zipo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Kipaumbele ni zile barabara ambazo zinaunganisha mikoa na mikoa, wilaya na wilaya. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Iringa Mjini kupitia Jimbo la Kalenga kwenda Kilolo kilometa 133 ambayo ina madaraja ni barabara ambayo ilikuwa ni ahadi ya hayati Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, alipofika pale akatoa ahadi hiyo, ni miaka mitano sasa imepita haijafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ni lini Serikali itaijenga barabara hii ili angalau kumuenzi hayati kwasababu alienda akaona wananchi wa kule wanavyohangaika katika kuuza mazao yao kwenda katika sehemu mbalimbali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii yenye urefu wa km. 133 iliyoko Mkoani Iringa na ambayo ni ahadi ya aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Mheshimiwa Hayati, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli naomba nimhakikishie kwamba Serikali haitaacha ahadi zote ambazo zimeahidiwa na Mheshimiwa Rais. Nataka nimhakikishie kwamba barabara zote ambazo zimeahidiwa na Mheshimiwa Rais ikiwa ni pamoja na hiyo zitajengwa kwa kiwango cha lami awamu kwa awamu. Ahsante.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa sababu, iko study ambayo ilifanyika enzi za mkoloni kwamba, kuna umuhimu wa kujenga reli kuanzia Tunduma kwenda Kasanga, lakini kwenda mpaka Ziwa Nyasa kwa maana ya Kyela na study hiyo iko NDC hadi leo ninavyoongea. Je, Serikali haioni umuhimu wa kufuatilia study hiyo ambayo ilifanywa na mkoloni na akaona viability ya mradi huo ili sasa ianze kutekeleza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa, Mheshimiwa Rais ambaye wakati ule alikuwa Makamu wa Rais, wakati amekuja kuomba kura kwa ajili ya CCM, katika mahitaji ya wananchi wa Mkoa wa Rukwa ilikuwa ni pamoja na ujenzi wa kipande hicho cha reli na akasema amepokea na ambaye leo ndio ndio Rais; na kwa kuwa mahusiano yetu na Serikali ya China hayana shida hata kidogo na kwa sababu, wao ndio walitusaidia katika ujenzi wa Reli ya TAZARA. Je, Serikali haioni umuhimu uleule ili tutumie window ya uhusiano mzuri na China ili vipande hivi viweze kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Josephat Sinkamba Kandege, Mbunge wa Kalambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, study aliyosema Mheshimiwa Mbunge ya mkoloni ni wazi kwamba haiwezi ikatumika kwa sasa. Kitakachofanyika inaweza kuwa tu ni kufanya review ya hiyo study kwa sababu, mazingira yamebadilika sana. Pia kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi ni kwamba, miradi hii ni miradi ambayo inahitaji fedha nyingi sana. Ikumbukwe tu kwamba, kwa sasa hivi kipaumbele cha Serikali ya Tanzania ni kujenga reli ya SGR Awamu ya Kwanza kutoka Dar-es-Salaam mpaka Mwanza ambayo nina hakika ikishakamilika tutakwenda na awamu nyingine. Kwa hiyo, kama Serikali hasa kwa kulingana na ufinyi wa bajeti, naamini hatuwezi kwenda na miradi yote miwili. Ndio maana nimesema upembuzi yakinifu utatuambia gharama ni kiasi gani, ili huo mradi uweze kuanza kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Kandege, Mbunge wa Kalambo ameeleza pia kwamba, Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba, ujenzi huu uweze kufanyika wa reli na ilikuwa ni ahadi. Nakubaliana naye na hatusemi reli hii haihitajiki kujengwa. Tunachosema ni kwamba, tutakwenda kwa awamu na study ndio itakayotuambia gharama iliyopo, lakini pia itazingatia na vipaumbele vya Taifa, tuanze nini tumalizie na nini. Ahsante.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa umuhimu wa reli hii ya kutokea Tunduma kwenda Kasanga unafanana kabisa na umuhimu wa barabara inayoanzia Mwandiga na kuelekea Chankere na inayopita nyuma ya Hifadhi ya Gombe na mpaka kwenda kwenye Bandari ya Kagunga. Je, Serikali haioni kuna umuhimu sana wa kuikamilisha barabara hii haraka iwezekanavyo kwa sababu, barabara hii ni barabara kwanza ya kiuchumi, lakini barabara hii pia ni barabara ya kiulinzi kwa sababu, ukanda huu hatuwezi kuwafikia wananchi wetu pasipo kupita nchi jirani ya Burundi. Je, Serikali haiwezi kututoa kwenye utumwa huu wa kupitia nchi jirani kwenda kuwahudumia watu wetu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa barabara maana anayoongelea ni Barabara ya Mwandiga – Chankere hadi Kagunga. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kusanifu barabara hiyo kwa sababu, barabara hiyo bado haijafunguliwa na tunajua kwamba, ni barabara muhimu sana kwenda Bandari ya Kasanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inatambua umuhimu wa barabara hiyo kuwahudumia wananchi wa Kagunga. Mheshimiwa Makanika amekuwa anafuatilia sana hii barabara, nimhakikishie kwamba, Serikali inalifahamu na nadhani pia, ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, hii barabara iweze kufunguliwa. Kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha kuona kwamba, barabara hii inafunguliwa. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya swali la nyongeza. Kwa kuwa, Serikali imejikita katika umaliziaji wa reli ya mwendokasi kwa jina lingine SGR kutoka Dar-es-Salaam awamu ya kwanza mpaka Morogoro na kutoka Morogoro mpaka Makutupora awamu ya pili; na kwa kuwa, TAZARA ni reli ya kimkakati na TAZARA inaanzia Mlimba inachepuka mpaka Kidatu. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuendelea na hiyo reli mpaka Kilosa kuungana na hii reli ya mwendokasi, ili kurahisisha usafirishaji wa mizigo kutoka reli ya kati na reli ya SGR kutoka Kilosa kuja Kidatu? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Denis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba, kuna umuhimu mkubwa sana wa kuunganisha reli ya SGR na reli ya TAZARA kuanzia Kilosa hadi Mikumi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Denis Londo kwamba, Serikali ina mpango huo wa kuziunganisha hizo reli, lakini upembuzi yakinifu utafanyika pale tu ambapo Serikali itakuwa imepata fedha, lakini tunaona kabisa ni muhimu kuziunganisha hizi reli kwa ajili ya ustawi wa uchumi wa nchi, lakini pia kuziunganisha hizi reli eneo la Kilosa na Mikumi. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Umuhimu wa reli ya kutoka Tunduma kwenda Kasanga ni sawa kabisa na umuhimu wa reli ambayo ilishakuwepo kabla ya Tanganyika kupata uhuru ya kutoka Mtwara – Nachingwea kwa Mikoa ya Kusini. Je, ni nini mpango wa Serikali wa kufufua reli ya Mtwara – Nachingwea mpaka Nyasa kwa manufaa ya kiuchumi na shughuli za kijamii kwa Mikoa ya Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Kasinge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbunge atakubaliana nami kwamba, Serikali ina mpango wa kujenga reli ya Mtwara hadi Mbamba Bay kwa kiwango cha SGR ambapo tayari upembuzi yakinifu umeshakamilika na usanifu wa awali umeshafanyika. Serikali imeshatafuta tayari transaction adviser kwa ajili ya kuandaa andiko ili kutafuta mbia ambapo reli hiyo tunategemea itajengwa kwa mfumo wa PPP. Kwa hiyo, itategemea na kama mbia huyo atapatikana haraka, basi hiyo reli itajengwa. Reli hiyo itahudumia corridor ya Mtwara kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay, lakini pia itakuwa na branch kwenda Liganga na Mchuchuma kwa ajili ya kusafirisha madini ambayo tunategemea yatazalishwa katika migodi hiyo. Ahsante.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na maelezo ya Naibu Waziri juu ya swali langu Namba 24, napenda kuuliza maswali ya nyongeza mawili kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ni uchumi, barabara ndiyo kila kitu. Swali hili naliuliza kwa mara ya pili katika Bunge lako tukufu lakini majibu ni yale yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza: kwa kuwa barabara hii kipindi cha mvua imekuwa hapitiki na ndiyo maana nimekuwa naomba muda mrefu kwamba barabara hii itengenezwe kwa kiwango cha lami, ni kwa sababu ni barabara ambayo ina uchumi wa hali ya juu sana; barabara hii ina ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete; kwa maelezo ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba bajeti haitoshi, fedha hakuna.

Je, wananchi wa maeneo haya ya Gairo na Kilindi ni liniwatarajie barabara hii kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: barabara hii ambayo ina magari mengi na shughuli nyingi za kiuchumi, ina madaraja au mito ya Chakwale, Nguyami na Matale; kipidi cha mvua haipitiki na Serikali kwa kweli imejitahidi mara kadhaa kujenga madaraja.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari sasa kutuma timu yake kwenda kukagua kuona hali halisi, kwa sababu barabara hii kwa sasa hivi haipitiki na wananchi wanapata adha kubwa? Ahsante.
NAIBU WAZII WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Kigua, Mbunge wa Kilindi kwa kuendelea kuwatetea wananchi wa Jimbo la Kilindi ili kuhakikisha kwamba wanapata barabara ya kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, barabara zote ni muhimu sana kwenye masuala ya uchumi, lakini pia katika kurahisisha usafirishaji wa bidhaa na usafiri wa wananchi. Ndiyo maana tuna ilani ya miaka mitano ambapo katika ilani hiyo tunaamini kwamba katika miaka mitano hatuwezi kutekeleza miradi yote kwa mwaka mmoja. Kwa hiyo, pamoja na kwamba ni kweli ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, nalo tunalijua. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi zitajengwa katika kipindi hiki cha miaka mitano mara tu fedha zitakapopatikana na katika bajeti tunazoendelea kuzitekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu barabara ya madaraja hayo matatu, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyoongea nimewasiliana na kutaka kupata changamoto za barabara hii. Wiki hii Meneja wa TANROADS wa Tanga na wa Mkoa wa Morogoro, watatembelea hii barabara na kuona changamoto ambazo zinaendelea katika haya madaraja ili tusije tukakatisha usafiri kati ya mikoa hii miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hilo suala litafanyika na Mameneja wote kwa sababu ni barabara inayounganisha mikoa miwili. Ahsante. (Makofi)
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara ya Nyamisati – Bungu ni muhimu sana kwa wananchi wa Wilaya ya Kibiti hasa wakazi wa Kata za Mwambao, Maege, Mlanzi, Waluke na Kata ya Salala.

Je, ni lini sasa Serikali itatenga fedha ili shughuli za awali za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ziweze kufanyika, barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Bungu – Nyamisati ni barabara ambayo inaunga kwenye barabara ya Dar es Salaam – Lindi – Mtwara na ambayo ina kilometa takribani kama 43 na bahati nzuri nimeitembelea barabara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni kati ya barabara muhimu sana kwa sasa kwa sababu ndiyo baada ya kujenga bandari ya Nyamisati na kuwa na kivuko ambacho kinafanya kazi kati ya Nyamisati na Mafia, kwa hiyo Wizara inatafuta fedha ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu sasa ndiyo barabara inayotumika sana na wananchi wa kutoka Kisiwa cha Mafia kuja Nyamisati na kwenda sehemu nyingine za Tanzania.

Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mpembenwe kwamba barabara hii tunatafuta fedha ili wananchi hawa waweze kufanya shughuli zao kwa uhakika zaidi na hasa tukizingatia kwamba ndiyo barabara muhimu inayounganisha watu wa Mafia na watu wa huku bara. Ahsante.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ujenzi wa barabara inayotoka Tabora Mjini kuelekea Mambali Bukene, imekuwa ikisuasua kwa muda mrefu. Barabara hii ilikuwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 – 2020 lakini mpaka sasa barabara hii imekuwa ikisuasua hivyo kusababisha wananchi wanaotoka Tabora kuelekea Shinyanga na Mwanza kupata usumbufu mkubwa kuzunguka:-

Je, Serikali inatoa ahadi gani kwa wananchi wa Tabora kuhusu barabara hii ili kurahisisha usafiri katika mikoa hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Bukene – Tabora ni barabara ambayo tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Ni barabara ambayo ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Kwa hiyo, tayari Serikali imeshaonesha commitment kwamba ni barabara ambayo iko kwenye mpango wa kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na vipindi vya bajeti, lakini bado tuna mpango wa miaka mitano wa kuzijenga hizi barabara. Kwa hiyo, wananchi wa Tabora na wote wanaonufaika na barabara hii wawe na uhakika kwamba barabara hizi zitajengwa kama zilivyoahidiwa na kama zilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
MHE. FESTO T. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kuuliza, changamoto ya barabara ya Kilindi – Gairo ni sawasawa kabisa na changamoto ya kutoka Isyonji Mbeya kuelekea Kitulo Makete, barabara ambayo ina urefu wa kilometa 97.6 na kwa muda mrefu imekuwa na changamoto wananchi wetu wa Makete wamekuwa wakipata changamoto.

Naomba kuuliza ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa sababu ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka mitano mfululizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Tuntemeke Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Sanga amekuwa anaifuatilia sana hii barabara ya Isyonje – Kitulo – Makete na ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete kwamba barabara hii iko kwenye mpango wa ujenzi wa kiwango cha lami, kwa hiyo, labda tusubiri bajeti itakapopitishwa nadhani tutapata majibu sahihi zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuweka maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napongeza kwa majibu mazuri Serikali kwa namna ambavyo wameweza kutolea majibu katika swali hili lakini barabara hii ya Kolandoto kwenda Mwangongo - Kishapu ikiwa na kilometa 53 imekuwepo katika mpango wa utekelezaji wa Ilani ya mwaka 2015/2020 lakini barabara hii haikuweza kutekelezwa katika kipindi hicho.

Swali, je, Serikali haioni umuhimu sasa pamoja na Ilani kuainisha kuwa barabara hii sasa itakwenda kutekelezwa katika mpango wa miaka mitano kwa maana ya 2020/2025 imeweka umuhimu wa kuhakikisha kwamba barabara hii sasa inatekelezwa tofauti na kipindi cha miaka mitano ambacho haikuweza kutekelezwa kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; barabara hii ni barabara ambayo ni trunk road ambayo kimsingi uchumi wake na uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Kishapu unaitegemea sana na hasa katika kusafirisha mazao kama pamba, mtama na mazo mengine, lakini barabara hii ni barabara ambayo itaenda kuunganisha takribani mikoa mitatu mpaka minne; Mkoa wa Simiyu, Mkoa wa Singida, hadi Mkoa wa Arusha ambako itapita Sibiti na Oldeani huko Arusha.

Naiomba Serikali itoe tamko na kuipa umuhimu barabara hii ili mradi iweze kuchochea na kuharakisha maendeleo katika mikoa hii. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Butondo, Mbunge wa Kishapu kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Butondo, lakini pia Wabunge wote ambao barabara hii inawahusu. Barabara hii ya Kolandoto – Mwingogo hadi Oldeani B ni kweli ni trunk road, kwa hiyo, Serikali inatambua umuhimu wake na ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote ambazo ni trunk roads zinakuwepo kwa kiwango cha lami. Katika jibu langu la msingi ambalo ni la utekelezaji wa Ilani ya mwaka 2015/2020 barabara hii iko kwenye mpango na tumesema maandalizi yanaendelea. Kwa hiyo, naamini kabla ya mwezi Juni tutakuwa tumeshaanza utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwenye Ilani ya mwaka 2020/2025 na kwenye mipango yetu naamini barabara hiyo bado itapata fedha kwa ajili ya kwenda kutekelezwa ili kuweza kurahisisha usafiri na usafirishaji kati ya mikoa hiyo ya Shinyanga, Simiyu, Singida na Arusha. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ambayo inaongelewa ya kwenda Kishapu ni sawasawa kabisa na barabara ya kilometa 60 ndani ya Mji wa Njombe yaani Ntoni na kwenda mpaka Lusitu. Barabara hii tunaambiwa ilishafanyiwa upembuzi yakinifu, imeshafanyiwa usanifu wa kina lakini sio tu hivyo, barabara hii vilevile imekuwa kwenye ahadi za Ilani ya Uchaguzi wa CCM ya mwaka 2015 - 2020 na mwaka 2020 – 2025.

Swali, ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara hii ambayo ni muhimu sana kiuchumi na inapita katika maeneo ya Njombe Mji, Uwemba, Luponde na Matola? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoisema atakubaliana na mimi kwamba iko sehemu ambayo ndiyo inakwenda mpaka huko Ludewa tayari imeshaanza kufanyiwa kazi na mimi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge awe na subira, kipindi hiki ni cha bajeti tunatambua umuhimu wa hii barabara na nadhani baada ya bajeti ataamini kwamba Serikali kweli ina mpango wa kuhakikisha kwamba barabara hii ya Njombe – Itoni – Lusitu inajengwa. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii iko kwenye mipango ya Wizara kwa maana ya Serikali kwamba itaendelea kujengwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na mimi naomba kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, uchumi wa Wilaya za Kilombero, Majimbo ya Kilombero, Mlimba, Wilaya ya Ulanga pamoja na Malinyi unategemea sana barabara ya kutoka Kidatu mpaka Ifakara kukamilika kwa ujenzi wa lami. Nakumbuka mkandarasi alishafanya mobilization, lakini kwa sababu ya changamoto za mgogoro wa kikodi limesimama.

Ni lini sasa Serikali inawahakikishia wananchi wa maeneo hayo kwamba tutaanza kujenga barabara hiyo kwa lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Humphrey Polepole, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ya Mikumi – Ifakara ni barabara ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami na mkandarasi anayeitwa Reynolds.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema, kulikuwa na changamoto za kikodi lakini pande zote zimeshakaa kwa maana ya Wizara, Wizara ya Fedha na mkandarasi na kwamba zile changamoto zilizokuwepo zimeondolewa na tunaamini muda sio mrefu barabara hii itaanza kujengwa na kwa maana ya kukamilika kwa barabara hii itakuwa imerahisisha sana wafanyabiashara na wananchi wa Wilaya alizotaja za Malinyi, Ulanga, Kilombero, Mlimba na hata Ifakara yenyewe.

Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba changamoto zilizokuwepo tayari Serikali na mkandarasi imeshakaa pamoja na imeziondoa na tuna hakika ujenzi utaanza mara moja ambao ulikuwa umesimama. Ahsante. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Wizara ya Ujenzi inataka kuunganisha barabara za mikoa kwa kiwango cha lami na kwa kuwa Serikali inatambua umuhimu wa kuzi- upgrade barabara zetu kuwa kwa kiwango cha lami kwa sababu itasaidia wananchi kusafirisha mazao, lakini wananchi wataweza kupata huduma bora za kupita kwenye barabara inayopitika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya kuunganisha barabara katika Mkoa wa Arusha ambayo inatoka Karatu kuunganisha Simiyu na inayotoka Karatu kwenda Mbulu kwa maana inaunganisha Arusha na Manyara.

Je, ni lini barabara hizi zitajengwa kwa kiwango cha lami kama ahadi inavyoeleza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara alizozitaja za Karatu – Simiyu – Mbulu – Manyara ni barabara muhimu na ni barabara za Mkoa na ni kipaumbele cha WIizara na Serikali. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi zimeshawekwa kwenye mpango kwa sababu zinatakiwa zijengwe, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kujenga hizi barabara kunahitaji fedha na tunapopata fedha ndiyo tunapoanza ujenzi.

Kwa hiyo, kwa kuwa zipo kwenye Mpango na fedha hizi zinategemea pia na mapato ambayo Serikali inapata ili iweze kuzijenga kwa hiyo kwa kuwa stadi zimeshafanyika, mara fedha itakapopatikana na tunavyotambua ni kipaumbele chetu barabara zote ni mpango wa Serikali zote zinazounganisha mkoa na mkoa, wilaya na wilaya ziwe kwa mpango wa lami, lakini hatutazijenga zote kwa wakati mmoja. Lazima tutaanza na barabara chache, tunafuata zingine mpaka tutakamilisha. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndani ya Jimbo la Kibamba ipo ahadi ambayo ndani ya Ilani ya miaka mitano mfululizo 2015/2020 na 2020/2025 ujenzi wa barabara ya Makabe – Msakuzi – Mpiji Majohe ikiungana na barabara ya Kibamba Njiapanda – Mpiji Majohe kwenda Bunju kupita Mabwepande. Lakini pia ikumbukwe barabara hii pia ni ahadi ya mwisho kabisa ya Mheshimiwa Hayati Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri kwamba ni kati ya ahadi za mwisho kabisa za Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Nadhani aliitoa wakati yuko kwenye ile stand na bahati nzuri nilikuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi ikishakuwa na Mheshimiwa Rais ni utekelezaji. Lakini atakubaliana nami kwamba ahadi aliyotoa isingekuwa rahisi kwamba tumeanza kuitekeleza, lakini ahadi ambayo tunaizingatia na tayari shughuli zimeshaanza kuona namna ya kuanza kutekeleza ile ahadi. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi kama zile zikishatolewa, kinachofuata ni utekelezaji na mimi nimhakikishie kwamba Serikali kupitia Wizara yangu hiyo ahadi tutaitekeleza. Ahsante.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri na Naibu Waziri, pia tunashukuru kwa ajili ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya matengenezo madogomadogo lakini matengenezo haya madogomadogo hayakidhi haja ya barabara hii kwani wakati wa mvua inaharibika kabisa na tunakosa mawasiliano kati ya mji mmoja hadi mwingine. Je, Serikali haioni kuna haja ya kutupa commitment ni wakati gani barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ili tutatue changamoto hii kabisa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alfred James Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara zote za changarawe ama za udongo na hasa maeneo ya mwinuko inaponyesha mvua huwa zinakuwa na changamoto ya kuondoka udongo ama changarawe. Commitment ya Serikali pamoja kutekeleza ahadi ya Rais na Waziri Mkuu tayari Serikali inatafuta fedha ili tuweze kufanya usanifu wa kina ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha na fedha ikipatikana barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimshukuru Waziri kwa majibu ya Serikali ambayo ameyatoa, lakini naiomba Serikali kwamba MV Kitunda ni kivuko ambacho kinawasaidia sana wananchi wa Lindi kuvusha magari na bidhaa mbalimbali na shughuli za kiuchumi zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa ninavyoongea kivuko kimesimama kwa muda wa wiki moja changamoto iliyopo injini Na.2 kwenye selecta valve kuna shida. Naiomba Serikali kusaidia kwa haraka kupatikana kwa valve hii ili kivuko kiendelee kufanya kazi na wananchi waendelee kutumia kivuko hicho.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Lindi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunatambua umuhimu wa kivuko hiki cha MV Kitunda na kutokana na umuhimu wake tayari Wizara kupitia TEMESA imeshapeleka boti na hata hivi kutokana kwa kweli na ufuatiliaji wa karibu sana wa Mheshimiwa Hamida, Mbunge wa Lindi Mjini, tumepeleka boti kwa ajili ya kusaidia changamoto ambazo zinajitokeza.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mbunge kwamba, kama tulivyoahidi kivuko hiki kitatengenezwa, lakini wakati kiko matengenezo boti hilo litaendelea kubaki hapo kwa ajili ya kusaidiana na boti la Halmashauri ya Lindi ili kuhakikisha kwamba eneo hilo halisimami kufanya kazi kati ya Lindi na Kitunda. Ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, mbali na majibu mazuri ya Serikali, kwa kuwa swali hili limeulizwa kwa muda mrefu, kuanzia katika Mkutano wa Tatu, ambapo Mheshimiwa Kiswaga na mimi Mbunge wa Sumve tuliuliza na tukapata majibu ya namna hii hii.

Je, Serikali haioni sasa umefika wakati wa kulifanyia kazi jambo hili na kuanza taratibu za manunuzi ili barabara hii ijengwe? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa ujenzi wa barabara hii unaendana sambamba/unaathiriana na ujenzi wa reli ya kiwango cha standard gauge kutokea Isaka kwenda Mwanza kwa sababu, barabara hii kwa usanifu mpya inapita eneo tofauti na barabara iliyopo inapita na reli hii ikishajengwa, ina maana hakutakuwa na njia tena ya kupita kutoka Kwimba kwenda Magu.

Je, Serikali haioni sasa umefika wakati iharakishe ujenzi wa barabara hii, ili kuepuka kufunga njia ya kutoka Kwimba kwenda Magu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kasalali Mageni, Mbunge wa Sumve kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa barabara hii tuliyoitaja kwa kiwango cha lami. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itajengwa na sisi kwa upande wa Wizara tayari tumeshakamilisha taratibu zote ili fedha itakapopatikana basi tuanze utaratibu wa kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa suala la barabara hii aliyoitaja kuingiliana na reli hii ya kisasa ya SGR, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, yote hayo yalizingatiwa kwenye usanifu na kwa hiyo, tumuhakikishie kwamba, hakutatokea hiyo changamoto anayoisema kati ya muingiliano wa hizo barabara na hiyo reli. Cha msingi tu avute subira kwamba wakati reli imeshaanza kujengwa hiyo ya SGR kati ya Isaka na Mwanza, lakini fedha ikipatikana mara moja pia barabara hii itajengwa ili basi hii miundombinu yote iende sambamba kuyafungua hayo maeneo. Ahsante. (Makofi)
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Katika hali halisi hiyo pesa iliyotengwa 1.5 kwa ujenzi wa barabara ya lami ni ndogo sana na upembuzi yakinifu umefanyika muda mrefu sana.

Je, Serikali haioni haja ya kuongeza pesa angalau hata kidogo, watutengenezee hata kilometa 30 tu, kwa mwaka huu, halafu na zile zitakazobakia waongoze pesa kwa mwaka ujao watutengenezee? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Ahmad Pathan, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hela iliyotengwa ni hela ndogo kulingana na urefu wa barabara, lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii fedha iliyotengewa ni fedha ya awali kwa ajili ya mobilization na kadri fedha itakavyoendelea kupatikana kwa jinsi Serikali itakavyopata, itazidi kuongezewa ili kujengwa kwa kiwango chote.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii inatakiwa ijengwe katika kipindi cha awamu yote hii ya miaka mitano. Kwa hiyo, kadri fedha itakavyoendelea kupatikana basi barabara hii tunahakika kwamba itajengwa yote kwa kiwango cha lami, kwa maana ya Masasi, Nachingwea hadi Liwale. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hii barabara siyo kwamba fedha Serikali hawana ya kujenga, ninachokiona hapa ni kwamba Serikali bado haijaamua kujenga hii barabara, kwa sababu zipo barabara zimefanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2018, mwaka 2017, mwaka 2016 zimeshajengwa na zingine zinajengwa. Lakini hii tangu mwaka 2014, ninaiomba Serikali iamue kwa maksudi kabisa kuikomboa Wilaya ya Liwale na Wilaya ya Nachingwea ili iweze kufunguka nasi kiuchumi tuweze kuwa miongoni mwa watu waliopo duniani.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja ya vitu ambavyo vinaongoza katika kutengeneza hizi barabara kwa kweli ni uwezo wa Serikali kwa maana ya bajeti, lakini Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ahadi za viongozi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Nachingwea - Liwale kwenye Ilani yetu ni kati ya barabara ambazo zipo kwenye usawa wa kilometa 7,500 ambazo zinatakiwa zikamilishwe usanifu wa kina kazi ambayo tayari imefanyika. Kwa hiyo ni hatua ya awali ambayo imefanyika na sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, usanifu tayari umekamilika kama ilivyoahidiwa kwenye bajeti mwezi Juni mwaka huu. Kwa hiyo, tayari Serikali imeshapiga hatua na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Liwale kwamba kwa kuwa tayari tumeshaanza kadri fedha zitakapopatikana naamini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Kuchauka ameonesha masikitiko yake makubwa kabisa, naamini nasi umetupa nafasi kwa maana ya Wabunge wa Nachingwea, Ndanda, Masasi na maeneo mengine kwenye umuhimu wa hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami nimuulize Mheshimiwa Waziri, Wizara imetenga shilingi bilioni 1.5 tu, kwa makisio ya sasa ni kama kilometa moja na nusu, wanapotaka kuanza kujenga barabara hii wataanzia kujenga upande gani? kwa sababu shida ipo Masasi, shida ipo pia Nachingwea. Watueleze wanataka kuanza kujenga upande gani kwa pesa kidogo namna hiyo waliyoitenga. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwambe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara tunachojenga ni kilometa hizo 45 kati ya Masasi na Nachingwea. Lakini hata ukianza Masasi, ukianza Nachingwea bado barabara ni ileile mtu atakapopita, atapita kokote. Nadhani nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba suala la kuanza wapi ama wapi nadhani isingekuwa ni hoja kubwa cha msingi tukamilishe hizo kilometa 45 kwa sababu hata kama itaanzia Masasi, itaanzia Nachingwea, lakini atakayepita, atapita tu kwenye hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, nadhani hilo aiachie Wizara na wataalam wataangalia pia wapi tunapofanya mobilization inaweza kuwa ni rahisi, jambo la msingi tukamilishe hizo kilometa 45. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyopo kule Liwale, Nachingwea yanafanana kabisa na yaliyopo katika Jimbo la Manyoni Magharibi Mkoa wa Singida kuunganishwa na Mkoa wa Mbeya kwa barabara inayotoka Mkiwa, Itigi hadi Rungwa.

Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Massare Mbunge wa Jimbo la Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba katika bajeti tuliyopitisha barabara hii ya kuanzia Mkiwa kwenda Rungwa, Lupa hadi Makongorosi, imetengewa bajeti kuanza kwa kiwango cha lami. Na sisi kama Wizara tunategemea muda wowote barabara hii iweze kutangazwa kwa ajili ya ujenzi, kwa sababu ni kati ya barabara chache ambazo zimebaki ambazo ni barabara kuu, trunk, yaani kuunganisha Mkoa wa Singida na Mkoa wa Mbeya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zote za manunuzi zimeshakamilika, tunachosubiri ni kutangaza hiyo tender kwa sababu fedha imeshapitishwa na Bunge lililopita kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na changamoto za kifedha kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameeleza lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo jibu la Waziri linasema ujenzi wa barabara hii baada ya Mkandarasi Mshauri kuwa amekamilisha kazi yake itategemea na upatikanaji wa fedha. Upatikanaji wa fedha ni kweli kwamba unaweza ukachukua hata zaidi ya miaka mitatu au minne. Swali langu la kwanza, kwa sababu barabara sasa hivi imekuwa na magari mengi takriban 2,000 kwa siku kutoka Nyegezi kwenda Usagara mpaka Mjini, Serikali itakuwa tayari angalau kuanza kwa hatua mbili; walau baada ya Mkandarasi Mshauri kumaliza itakuwa tayari kuanza kujenga hata kwa km 10 kwa phases na baadaye km 10?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, wako watu kutoka Kata ya Nyegezi na Mkolani ambao wameongezeka zaidi ya mita 7.5 kwenye barabara hii na watu hao wanastahili kulipwa fidia. Je, Serikali itakuwa tayari kuwalipa fidia stahiki kwa sababu za msingi ili barabara hii iweze kujengwa bila vikwazo na wananchi wapate huduma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, usanifu wa kina utakamilika Septemba na baada ya hapo barabara hiyo itaanzwa kujengwa kwa kiwango cha lami. Kuhusu upatikanaji wa fedha na ni kwa kiasi gani tunaweza kujenga, matarajio ya Serikali ni kukamilisha barabara lakini tutaanza kadri fedha itakavyopatikana ndiyo tutaanza kujenga kama ni km 5, km10 ama ikiwezekana zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu fidia, hatutajenga bila kufanya tathmini na ndiyo maana ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ambao unachukua masuala yote; kuangalia ni kiasi gani cha fedha kinatakiwa ili wananchi wa Kata za Buhongwa na Nyegezi ambao wameongezeka sana watafidiwa. Ni utaratibu kwamba ni pale ambapo wananchi wa Kata za Buhongwa na Mkolani watakapokuwa wamefidiwa ndipo ujenzi utaanza. Ahsante.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Bunge lililopita la Kumi na Moja, Bunge lako Tukufu lilielezwa kwamba Serikali imetenga shilingi bilioni 5 kuanza kuweka lami barabara ya kutoka Same Kisiwani - Mkomazi. Je, kazi hii itaanza lini? Ahsante (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Naghenjwa Kaboyoka, Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama Serikali ilivyoahidi kwamba imetenga shilingi bilioni tano kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Same Kisiwani, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba bado barabara nyingi hazijatangazwa na zitaendelea kutangazwa kadri tunavyokwenda na barabara nyingi tu zitatangazwa kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha. Pia tunategemea baada ya bajeti hii barabara hizo zitaendelea kujengwa ikiwa pengine ni pamoja na hii Same Kisiwani, itategemea na bajeti hii tunayoendelea kuipitisha itakavyokuwa imepita. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati DKt. John Pombe Magufuli, alivyokuwa Karagwe aliahidi kwamba watu wa Kyerwa watajengewa barabara kilomita 50 kwa lami. Hii barabara ya lami inahitajika kweli kwa sababu imekuwa ni mgogoro wa wananchi, je, itaanzia wapi hiyo kilomita 50 ya lami? Licha ya kuahidiwa bado ujenzi huo haujaanza. Swali, ni lini hizo kilometa 50 tulizoahidiwa na Mheshimiwa Rais zitaanza kujengwa hata ikibidi tukaongezewa zikawa hata 100? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ahadi zote za Viongozi wa Kitaifa tunazizingatia na huwa tunazitekeleza. Ahadi ikishatolewa kuanza kwa barabara si kuingia site na kuona magreda yanaanza kutembea lakini barabara itafanyiwa usanifu na usanifu wa kina ndipo itakapoanza kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la pili barabara itaanzia kujengwa wapi, sisi kama Serikali kokote tukianzia ili mradi kilomita 50 zitatimia tutaijenga barabara hiyo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na taratibu za kutimiza ahadi za Viongozi wa Kitaifa ikiwa ni pamoja na barabara hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja kwamba zitajengwa kama zilivyoahidiwa na Kiongozi wetu wa Kitaifa. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Umuhimu wa barabara ya Kenyatta katika Halmashauri ya Jiji la Mwanza ni sawa kabisa na umuhimu wa barabara ya kutoka Kiranjeranje - Nanjilinji mpaka Ruangwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, Jimbo la Kilwa Kusini. Lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ni kati ya barabara ambazo zimeainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ni barabara ambayo pia imeahidiwa na viongozi wa Kitaifa. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri fedha itakapopatikana barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami mara baada ya kukamilisha usanifu wa kina wa barabara hii. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Hai. Mgogoro huu umekuwa wa muda mrefu sana, jambo linalosababisha wananchi kukosa maeneo ya malisho na kuishi kwa wasiwasi kwenye maeneo yao ambayo wanaishi pale tangu mwaka 1975. Wananchi wote wa vijiji hivi vyote vinne vinavyotajwa, wana usajili wa vijiji vyao, nikimaanisha Kijiji cha Sanya station, Tindigani, Mtakuja na Chemka.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, ukizingatia eneo lililopo kwenye uwanja huo ni kubwa sana; kwenye list ya Viwanja vya Ndege tulivyonavyo hapa Tanzania, Kiwanja cha Kilimanjaro Airport kinaongoza kikifuatiwa na Kiwanja cha Dodoma na Songwe, halafu kiwanja cha nne ni Dar es Salaam.

Je, Serikali haioni kwa ukubwa ulioko pale, iko haja ya baadhi ya maeneo yarudi kwa wananchi ili waweze kuendelea na maeneo yanayobaki, yabaki kwenye Uwanja huu wa Ndege jambo ambalo tayari mimi mwenyewe nilishakutana na Management na wakaonyesha utayari wa kukubaliana na jambo hili?

Swali la pili: Je, Kwa kuwa mgogoro huu umekuwa wa muda mrefu, Serikali haioni iko haja sasa wa kufikia mwisho na Mheshimiwa Naibu Waziri sasa tuambatane tukakae na wananchi wale tumalize mgogoro huu ili kesi hii iishe na wananchi waendelee na maisha yao; na kwa kuzingatia kwamba wananchi hawa ni wema sana, walitupa kura nyingi za Chama cha Mapinduzi na pia Diwani aliyeko pale alipita bila kupingwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mgogoro huu umekuwa ni wa muda mrefu na hapo nyuma kulikuwa kuna changamoto kwamba vijiji vilipima maeneo yao yakaingia katikati ya uwanja ambao tayari ulikuwa una hati. Changamoto hiyo tayari tulishairekebisha na zile ramani za vijiji vile zilifutwa ili ramani ya uwanja wa ndege ibaki na ndivyo ilivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa ni kweli kwamba uwanja ule ni mkubwa lakini uwanja ule ulitolewa vile na muasisi wa Taifa baba yetu Julius Kambarage Nyerere na kile kiwanja kina mipango mahsusi ya kuweka viwanda vya kitalii na viwanda vinavyohusiana na viwanja vya ndege. Biashara zote za viwanda vya ndege, sasa hivi pale kuna mpango wa kuanzisha aviation school ambapo Chuo cha Taifa cha Usafirishaji kimekwishajidhatiti na vile vile tuna mpango na hawa watu wa TAA ili kuweka majengo ya kuhifadhi mipango ambayo imepangwa pale. Kwa hiyo ningependa kumshauri Mheshimiwa Mbunge pamoja na wale wananchi wa Hai wajipange kuanzisha biashara zinazohusiana na viwanja vya ndege kuliko kupanga kuugawa uwanja wa ndege ule kwenda katika vijiji.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni kweli kwamba Wizara yangu iko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kwenda pale kuongea na kumaliza suala hilo kwani tumejipanga mwaka huu tuweze kufika pale kufanya tathmini na kumaliza suala hilo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO Mheshimiwa Spika nashukuru kwa majibu ya Serikali, na niwapongeza Serikali kwa kuanza kufanya mradi huu kwa kuweka taa za barabara kuu za Mji wa Maswa. Ninachosikitika ni kwamba mradi huu umekwenda nusunusu sasa naomba Mheshimiwa anipe majibu ya kweli wameweka taa 18

Je, wana mpango wa kuweka taa ngapi ambazo zitatosha kuanzia Mwigumbi kwenda njia panda.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wananchi wa Maswa wanapata shida barabara hiyo zinapopita gari kwa kasi kubwa watu wanapata ajali na wengine wanapoteza maisha na kuna mpango wa kutengeneza bypass road kuzunguka Mji wa Maswa.

Je, barabara hiyo nayo itajengwa lini? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba katika barabara zote za sasa ambazo zinatengenezwa imekuwa ni sehemu ya mkataba kwamba pale ambapo barabara zinapita kwenye Miji, moja ya eneo ambalo lazima lishughulikiwe na Wakandarasi ni kuweka taa za barabarani ikiwemo Mji wa Maswa. Taa sizopungua 60 zitaweka katika Mji wa Maswa ili kukamilisha Mji wote kwenye barabara ile kuu, swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, bypass road ya Maswa itajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha ipo kwenye mpango na itajengwa mara tu Serikali itakapokuwa imepata fedha ahsante.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika nashukuru kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara ya Maswa ina umuhimu sana sawasawa na barabara ya watu wa Kibiti kutoka Kibiti Dimani kwenda Mloka kule ambako kuna ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere, na kwa kuwa Mheshimiwa Rais mama yetu Samia wakati anainadi ilani ya Chama Cha Mapinduzi aliahidi kwamba barabara ile itajengwa kwa kiwango cha lami.

Je, ni lini Serikali itatenga fedha ili shughuli za awali za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina zianze mara moja katika barabara hiyo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Kibiti ni moja ya barabara muhimu sana ambayo ni moja ya njia inayofika kwenye Bwawa la Nyerere, na barabara hii ni ahadi ya viongozi wetu wa Kitaifa.

Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Kibiti, kwamba barabara hii ipo kwenye mpango na itajengwa kwa kiwango cha lami kama viongozi ambavyo wametoa ahadi na kama ambavyo inaonekana kwenye ilani ya Chama Cha Mapinduzi ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Msalala, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara hii imekuwa kero kubwa sana kwa wananchi, hususan wa Kata za Segese, Shilela, Ngaya na Bugarama. Barabara hii imeahidiwa kiasi cha dola milioni 40 kwa ajili ya kutengenezwa na Mgodo wa Barrick na imekuwa ni kero kubwa sana kwani inasababisha wakazi wa maeneo haya ambayo nimeyataja kuhama makazi yao asubuhi na kurudi jioni kutokana na vumbi kali kwa sababu inatumiwa na magari makubwa. Je, ni lini sasa Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Madini watakwenda kwa Waziri wa Fedha ili wamwambie Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweze kutekeleza mkataba na makubaliano walioingia baina ya Serikali na Mgodi ili Mgodi uanze kutengeneza barabara hii mara moja? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni lini sasa Serikali itaanza kufikiria ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara inayotoka Kahama kupita Kata ya Busangi kwenda Nyang’hwale na kutokea Busisi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kassim Iddi Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Msalala kwamba katika jibu langu la msingi nimesema Mgodi wa Barrick wameonesha nia maana yake ni kwamba tayari timu ya majadiliano imeundwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na Wizara ya Madini, lakini kwa sababu tunayojadili ni masuala ya fedha timu hiyo imejuimuisha pia Wizara yenyewe ya Fedha. Kwa hiyo, once majadiliano yatakapokuwa yamekamilika na kupata utaratibu sahihi, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo itaanza kujengwa ili kuwapunguzia adha wananchi wake wa Lunguya, Segese, Ntobo hadi Bukoli na Geita ambao wako Mkoa wa Geita. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge aamini kwamba Serikali itafanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Nyang’hwale kwenda Busisi, naomba pia nimhakikishie kwamba ipo kwenye mipango, ipo kwenye Ilani na tuna mpango wa miaka mitano ambao nina hakika katika kipindi hiki barabara hiyo pia itajengwa kadiri fedha zitakavyopatikana. Ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, Dkt. John Pombe Magufuli, alipopita kwenye Jimbo letu la Morogoro Kusini Mashariki alituahidi barabara ya Bigwa – Kisaki. Naomba kuiuliza Serikali barabara hii itaanza lini kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Babu Tale, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli alipotembelea Mkoa wa Morogoro, moja ya ahadi alizotoa na ilikuwa ni maagizo kwamba barabara hii ijengwe haraka kwa kiwango cha lami. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Babu Tale, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki na wananchi anaowaongoza wa Jimbo lake kwamba barabara hii kwa maelekezo ya Mheshimiwa Waziri itajengwa kwa kiwango cha lami kuanzia kilometa 50. Kama navyoongea naye mara kwa mara, nimhakikishie kwamba barabara hii itakuwa ni kati ya barabara ambazo zitatangazwa muda si mrefu kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri juu ya ujenzi wa barabara hiyo, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa Serikali imeshafanya upembuzi yakinifu wa kilometa hizo 100 ambazo zinatokea Makofia kuendelea Kisarawe, je, ni lini Serikali italipa fidia wananchi hawa ili kupisha ujenzi huo uendelee kwa sababu ni wa muda mrefu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa barabara hii; na kwenye majibu yake anakiri kwamba ametenga pesa ya kufanyia ukarabati wa muda wakati wakisubiri tukipata pesa, naomba niifahamishe Serikali kwamba kwa sasa barabara hii haijafanyiwa ukarabati huo kwa miaka mingi. Kwa kuwa pesa hizi zimepangwa mwaka huu wa bajeti, je, Serikali haioni sasa ni muda sahihi kutafuta fedha za haraka kuzifanyia ukarabati barabara hizo kwa sasa kwani kipande cha kutoka Mlandizi kwenda Mzenga kina mashimo makubwa utadhani mabwawa ya kuvulia samaki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kila hatua inayofanyika ndiyo ujenzi wenyewe wa barabara ya lami unavyoendelea. Barabara hii haitaanza kujengwa mpaka kwanza fidia ya wananchi hawa ambao bahati nzuri tayari wameshatathminiwa watakapolipwa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mwakamo kwamba wananchi hawa watalipwa fidia pale tu ambapo Serikali itapata fedha. Jitihada kubwa zinafanywa na Serikali kuhakikisha kwamba tunapata fedha ili tuweze kuwalipa hao wananchi ambao tayari wameshaainishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili kwamba barabara hii haijafanyiwa matengenezo; naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kupitia Bunge hili naomba kumuagiza Meneja wa Barabara Mkoa wa Pwani aweze kutembelea barabara hiyo na kuangalia upungufu uliopo aweze kuikarabati kwa sababu fedha imetengwa ili wananchi waendelee kupata huduma ya barabara hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi. Pamoja na majibu ya Naibu Waziri, naomba kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, hali ya barabara ni mbaya sana kwa wananchi wa Wilaya ya Songwe na hali hii imesababisha wananchi kupoteza maisha, ikiwa ni pamoja na kuzikosa huduma za muhimu na za msingi ambazo wanatakiwa kuzipata katika Ofisi ya Mkoa. Je, Serikali haioni umuhimu wa kulichukulia jambo hili kwa dharura, ili wananchi waweze kuepukana na changamoto ambayo imekuwa ikiwakabili kila mwaka katika Wilaya ya Songwe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara anayoisema mwaka huu ilikuwa imesimama kwasababu ya mvua nyingi ambayo inaendelea kunyesha. Na kuna daraja linalounganisha Kijiji cha Tanga na Mbala ambapo mto ulitoka kwenye njia yake ukakata barabara na ukawa umetengeneza bwawa.

Mheshimiwa Spika, tunavyoongea na hasa kupitia Mbunge Mulugo wa Jimbo la Songwe tumekuwa mara nyingi tunawasiliananae na anafahamu fika kwamba, hadi sasa wakandarasi wako site. wameanza Alhamisi ya wiki iliyopita, tumapata fedha shilingi milioni 700 kwa ajili ya kukarabati batabata hiyo na kurejesha mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya hiyo barabara kukatika kuna barabara nyingine ambayo walikuwa wanapitia sasa Chunya – Mbeya kwenda Songwe. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, suala hilo lipo na tayari wakandarasi wako site na milioni 700 ziko tayari kwa ajili ya kuendesha mawasiliano ya barabara. Ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona, kwa kuwa, changamoto ya barabara ya Mbalizi – Mkwajuni inafanana kabisa na changamoto ya barabara inayoanzia Sepuka – Ndago hadi Kizaga. Na barabara hii tumekuwa tukiiulizia mara kwa mara, lakini tunaambiwa ipo kwenye upembuzi yakinifu. Je, ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami, ili kuchochea maendeleo ya Wilaya ya Ikungi pamoja na Wilaya ya Iramba? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Aysharose Matembe ambaye kwa kweli mara nyingi amekuwa akifuatilia, si tu barabara hii ya Sepuka – Ndago hadi Kisanga, lakini amekuwa akifuatilia barabara nyingi za Mkoa wa Singida.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, hizi barabara ni kati ya zile barabara ambazo zimeainishwa kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi kwa ajili ya kukamilisha upembuzi yakinifu, lakini pia na usanifu wa kina, ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge avute Subira tupitishe bajeti tuone kama hizi barabara zitakuwa ni kati ya ambazo tutaanzanazo kwa mwaka huu. Ahsante sana.
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Najua barabara yote kilometa 40 ina umuhimu mkubwa, lakini kipande katikati ya Kisiwani na Kibaoni ndiyo kipande hasa ambacho kina matatizo makubwa, Je, Serikali ina mpango wowote wa kukishughulikia kipande hiki kwa namna ya kidharula ili kuhakikisha kwamba kinapitika wakati wote wa mwaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwinjuma, Mbunge wa Muheza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi, barabara hii inaendelea kutengenezwa. Jana nimepita maeneo ya Tanga na nilikuwa na Meneja wa TANROADS na moja ya maelekezo ambayo tumempa ni kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo yana shida likiwepo hili la kati ya Kisiwani na Kibaoni wahakikishe kwamba wanapeleka nguvu zao ili pasije pakatokea tatizo la kutokuwa na mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa sababu barabara hii ipo kwenye matengenezo ndiyo maana tumeendelea kutenga hizo shilingi milioni 600 kwa ajili ya kurekebisha sehemu zozote ambazo ni korofi ikiwemo pamoja na hili eneo kati ya Kisiwani na Kibaoni. Ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yanayoleta matumaini makubwa kwa wananchi wa Jimbo la Kwela naomba nitoe alert kwa Serikali, mtaalam wa upembuzi yakinifu ambaye yupo site speed yake ni ndogo sana. Niombe tu close follow-up kuhakikisha anamaliza kazi hiyo ndani ya kipindi cha mkataba.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza; kwa kuwa barabara ya kutoka Mji Mdogo wa Laela kupitia Mnokola, Mwimbi mpaka kuunganisha nchi jirani ya Zambia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais alipokuja kwenye kampeni. Wananchi wa maeneo ya Kata hizo zilizopo pembezoni mwa barabara wamekubali kuachia reserve ya barabara ili ijengwe kwa kiwango cha lami kwa sababu ni muhimu kwa uchumi wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla. Naomba kupata commitment ya Serikali ni lini barabara hii itafanyiwa upembuzi yakinifu ili baadaye iweze kujengwa kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alipofanya ziara Mkoa wa Rukwa aliahidi ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka katika Kijiji cha Kaengesa - Seminari ya Kaengesa - Kitete kilometa saba na tayari upembuzi yakinifu umekamilika. Ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kuwa wananchi wanaisubiria kwa hamu na wanataka sana kuipata hiyo barabaa ya lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deus Sangu, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tumechukua ushauri wake na tutahakikisha kwamba TANROADS wanamsimamia mkandarasi ili aweze kukamilisha usanifu wa kina unaoendelea ndani ya mkataba.

Mheshimiwa Spika, maswali yake mawili ya barabara ya Lahela kwenda nchi jirani lakini pia Kaengesa kwenda Kitete kilometa saba, kama alivyosema hizi ni ahadi za viongozi wetu wa Kitaifa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo la Kwela, tumesikia na huo ndio ukweli kwamba ahadi zote zilizoahidiwa na viongozi wetu wa kitaifa zitaendelea kama zilivyoahidiwa. Kwa hivyo, Mheshimiwa Mbunge aelewe kwamba tunapoanza upembuzi na usanifu tayari ni hatua ya utekelezaji wa ahadi hizo. Tukishakamilisha basi nimhakikishie kwamba barabara hizo zitajengwa kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha kama viongozi wetu wa kitaifa walivyoahidi. Ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa barabara hii imekuwa ikipata ahadi nyingi sana za Serikali hasa kila wakati wa Uchaguzi mwaka 2015 imeahidiwa haikujengwa na leo inaahidiwa tena ndani ya Bunge lako Tukufu, wananchi wa Lupembe wanapenda kujua kuna utofauti gani wa ahadi za nyuma ambazo hazikutekelezwa na ahadi hii ya leo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Serikali ina mpango gani wa kuwalipa fidia wananchi ambao wataathirika na barabara hii hasa katika maeneo ya Nyombo, Kidegembye, Matembwe, Lupembe Barazani, Igombola, Mfiriga mpaka Madeke? Ahsante
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi za Serikali si za kubahatisha na namuomba nimuhakikishie kwamba ahadi ninayomwambia leo ni ahadi ya ukweli, awasiliane na uongozi wa TANROADS watamweleza wako kwenye taratibu za mwisho kabisa kutangaza hii barabara hizi kilomita 50 ili zianze kujengwa kwa kiwango cha lami na hasa tukitambua ni barabara ambayo inaunganisha mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro kupitia Mlimba Ifakara hadi Mikumi. Kwahiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge.

Swali lake la pili ni kuhusu fidia ni kweli tathmini ilishafanyika watu walishatambuliwa na gharama za ulipaji wa fidia ulishahakikiwa nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wananchi wote wa vijiji na kata alizozitaja watalipwa fidia yao kabla ya ujenzi kuanza. Hili litakwenda sambamba wakati ujenzi utakapokuwa unaanza wanafanya mobilization Serikali itakuwa inaendelea na kuwalipa ama kuwalipa fidia wananchi ambao watakuwa wameathirika na mradi huu ahsante.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nakushukuru mvua hizi zinazonyesha nchi nzima zinanyesha nazo Dar es Salaam hali ya barabara za Dar es Salaam ni mbaya na nikisema ni mbaya uchumi wa Dar es Salaam ukianguka ni uchumi wa Taifa unaanguka mapato ya Dar es Salaam ndiyo yanasaidia kujenga nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara za Jimbo la Ilala leo Kariakoo haipitiki, Upanga haipitiki, Soko la Ilala halipitiki wananchi wanauza bidhaa zao sasa barabarani. Mwarobaini ni pamoja na mradi wa DMDP II kuweza kupitishwa haraka kusaidia wakazi wa Dar es Salaam na hasa Jimbo la Ilala.

Sasa naiomba Serikali lini sasa Serikali itaanza kutekeleza mradi huu ambao tayari umeshawasilishwa na TAMISEMI menu yote ya mahitaji ya barabara ipo tayari Hazina ni lini Serikali inatoa kauli kwa mradi huu unaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika majiji yetu tuna barabara za aina mbili ziko barabara ambazo ni kweli zinasimamiwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi lakini tunasaidiana na Wizara ya TAMISEMI kwenye baadhi ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba kumekuwa na changamoto nyingi hasa kipindi cha mvua pale ambapo barabara zetu nyingi zinakuwa zimekatika lakini kama Mheshimiwa Zungu alivyosema Mbunge wa Ilala tayari upo mpango wa kuzitengeneza barabara hizi zikiwepo barabara zote za Majiji ya Dodoma Jiji la Mbeya, Jiji la Arusha na hata Jiji la Mwanza. Pengine rai yangu kubwa kwa wananchi ni kuhakikisha kwamba mengi ya matatizo tunayopata ni kwasababu aidha tumejenga kwenye mikondo ya maji kwa hiyo tunabadilisha mwelekeo wa maji. Lakini wakati fulani pia mifereji hii haisafishwi na kusababisha maji yanajaa na hivyo kutoka kwenye mikondo yake ya kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuhakikishie Mheshimiwa Zungu tuna mpango kabambe kama Serikali wa kuhakikisha kwamba suala hili tunalifanyia mkakati wa kudumu ili tuweze kuachana na hii adha kati ya Wizara ya Ujenzi na Wizara ya TAMISEMI ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nishukuru kwa Serikali kuzitamka barabara hizi lakini kwa namna majibu yalivyosemwa yanatofautiana kabisa na uhalisia ahadi hizi zilitolewa na Mheshimiwa Rais Samia Hassan Suluhu mwaka jana. Ujenzi wa kilomita nne unazosema ulijengwa miaka ya nyuma sana, nikiri mwaka jana kulikuwa na ukarabati wa eneo korofi kama mita chache sana siyo ujenzi. Sasa swali langu la msingi lilikuwa lini tutaanza kutekeleza lini Serikali itaanza kutekeleza ahadi hizi zilizotolewa na Mheshimiwa Rais wetu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili Serikali ilitoa ahadi hapa kwamba tutaanza kujenga barabara ya Kitai hadi Kigonsera kilomita tano juzi nimepita pale hakuna kilichofanyika wananchi wananiuliza. Je, Serikali mnawaambia nini wananchi wa Jimbo hili la Mbinga Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni wazi kwamba ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais wakati huo akiwa Makamu haingekuwa imeanza kutekelezwa lazima itaanza kutekelezwa katika awamu hii ya bajeti tunayoiendea.

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge uvute subira lakini kama tulivyosema ahadi hizi zote ambazo zimeahidiwa ni ahadi ambazo zinatakiwa zitekelezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusu barabara ya Kitai, Litui barabara hii ni kati ya barabara za kimkakati ambayo inaenda inapita kwenye makaa ya mawe ya Ngaka na atakubaliana nami Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari kilometa tano zimeshajengwa na naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba muda si mrefu kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha barabara hiyo tena inaendelea kujengwa itatangazwa mapema sana kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha na kwa kuhakikishia Mheshimiwa Mbunge unaweza ukawasiliana na TANROAD watakuambia taratibu wako kwenye hatua za mwisho kabisa ili mkandarasi aanze kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lako kwamba barabara zilijengwa muda wa nyuma ndiyo mpango wenyewe kwamba tayari tulishaanza kujenga na kwa hivyo tayari hizo kilomita tano tunazitambua tulizijenga na bado tutaendelea na hasa baada tena ya Mheshimiwa Rais kuongezea ahadi yake.

Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Mbinga wafahamu kwamba barabara zao zitajengwa kwa kiwango cha lami kama Serikali ilivyoahidi na kama ilivyo kwenye mpango ahsante.
MHE. SILLO D. BARAN Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini pamoja na majibu hayo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umeshakamilika, je, ujenzi wa barabara hii unaweza ukaanza kwenye bajeti ijayo ya mwaka 2021/2022? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pilli, kwa kuwa barabara hii inafanana na barabara ya Magugu kwenda Mbuyu wa Ujerumani kupitia Daraja la Magara ambalo limejengwa na Serikali kwa thamani ya shilingi bilioni 13 hadi Mbulu; je, Serikali ipo tayari kuanza ujenzi wa barabara hii pia ili kuchochea maendeleo katika eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sillo Baran, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Dareda hadi Dongobesh yenye urefu wa kilometa 54 kwenye maeneo ya escarpment ambayo tulijua yana changamoto yameshajengwa kilometa 10. Pia tumekamilisha usanifu wa kina mwaka huu, kwa hiyo, tusubiri bajeti; siwezi nikasema sasa hivi lakini nadhani litajitokeza kwenye bajeti lakini kwa maana ya kukamilisha usanifu wa kina maana yake tuna mpango wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami na hiyo tu ni hatua za kuelekea huko.

Mheshimiwa Spika, ameuliza barabara inayoanzia Mbuyu wa Mjerumani hadi Daraja la Magara. Barabara hii pia ipo kwenye mpango na itakamilika kufanyiwa usanifu wa kina Septemba mwaka huu. Kwa hiyo, tayari pia ipo kwenye mpango kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya kuanzia Mombo - Soni - Lushoto ni nyembamba mno na husababisha usumbufu mkubwa sana kwa watumiaji wa barabara hiyo hasa katika kipindi hiki cha mvua.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua barabara hiyo ya Mombo - Soni - Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara ya Mombo - Lushoto ni nyembamba. Nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi barabara hii itakapoingia kwenye mpango wa kuikarabati upya na ujenzi mpya tutaiangalia; ndio maana kunakuwa na usanifu mpya. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itakapoingizwa kwenye mpango wa kuijenga upya itafanyiwa Design upya na itapanuliwa ili kuweza kuingia kwenye viwango vya sasa vya barabara za mita saba na nusu kama zilivyo barabara nyingine. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kama unavyojua changamoto ya barabara mikoani ni kubwa na kwa Mkoa wa Mara katika miaka zaidi ya mitatu, minne TANROADS Mkoa wa Mara imekuwa haipewi fedha za kutosha kwa ajili ya ukarabati wa barabara. Sasa tunauliza ni lini Serikali itapeleka fedha za kutosha TANROADS Mkoa wa Mara ili iweze kukarabati barabara zote za Majimbo 10 ya Mkoa wa Mara ikiwepo Bunda Mjini; barabara ya kutokea Sazira – Nyamswa; barabara ya kutoka Kinyambwiga kuja Rwagu kutokea Ng’ombe mpaka Manyamanyama? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mgao wa fedha za TANROADS, fedha zinagawiwa sawa na hakuna upendeleo unaofanyika na Serikali kwenye barabara zake zote za Mikoa mbalimbali. Nataka tu nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna miradi kadhaa kwa kiwango cha lami ambayo mpaka sasa hivi inatekelezwa katika Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mbunge kwamba tunatoa fedha kwa usawa na hasa kwa miradi ambayo inatekelezwa na yeye ni shahidi zipo barabara za Nyamuswa, Bunda zinajengwa. Kwa hiyo, hatuwezi tukakamilisha miradi yote kwa wakati mmoja, lakini ni mpango wa Serikali kwamba barabara zote ambazo zimeainishwa kwenye Ilani na zimeahidiwa na viongozi zitajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Majibu ya Serikali kupitia Waziri hayaoneshi matumaini kwa wananchi wetu wa Ulyankulu kwamba wanaenda kupata lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilikuwemo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi 2015/2020 lakini pia kwenye Ilani ya Uchaguzi ya 2020/2025 barabara hii imo. Majibu ya Serikali yanaonesha barabara hii kwa kipindi chote hicho itakuwa tu kwenye upembuzi yakinifu.

Je, kwa miaka hii mitano mingine barabara hii ina uhakika wa kutengenezwa ili wananchi wangu waweze kupata barabara ya lami? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ni kwamba Hayati Dkt. John Pombe Magufuli alipotembea Jimboni kwetu Ulyankulu alitoa ahadi ya kututengenezea kilometa tatu kwenye Jimbo letu la Ulyankulu. Lakini tangu kipindi hicho mpaka leo hakuna hata kilometa moja iliyotengenezwa kwa kiwango cha lami.

Swali langu ni je, kupuuzwa kwa kutekeleza kwa kujengwa kwa hii barabara kwa hizo kilometa tatu ni kupuuza ahadi ya Mheshimiwa Rais au na kuwadharau wananchi wake waliompigia kura? Naomba majibu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Migilla, Mbunge wa Ulyankulu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Migilla kama amenisikiliza kwenye jibu langu la msingi ni kwamba tayari usanifu wa kina unaendelea na utakamilika Septemba mwaka huu. Barabara haiwezi ikaanza kujengwa kabla ya kukamilika kwa usanifu. Atakuwa ni shahidi kwamba wakandarasi wanaofanya usanifu wako field na Wizara inatambua kwamba barabara anayoitaja ni barabara muhimu sana kwani katika Jimbo lake tunatambua lina uzalishaji mkubwa sana wa mazao kama mahindi, mpunga na hata tumbaku.

Mheshimiwa Spika, hii barabara sasa ndiyo inayokwenda kwenye mbuga ambazo zimetambuliwa kama National Park ya Ugalla na nimhakikishie kwmaba katika bajeti ya mwaka ujao pia tumetenga fedha kwa ajili ya kufungua na kuanza ujenzi wa Daraja la Ugalla ili kuunganisha Jimbo lake na Mkoa wa Mpanda. Ni barabara ambayo tayari wakandarasi wapo wakiwa wanaifungua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimalizie kwa kumhakikishia Mheshimiwa Migilla haitatokea na haiwezekani Serikali hii ikapuuza ahadi za viongozi wetu wa Kitaifa. Ahadi imeahidiwa mwaka uliopita isingekuwa rahisi tuwe tayari tumeshajenga hizo barabara na ndiyo maana tunasema tayari wakandarasi wako site wakifanya usanifu wa kina.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge barabara hiyo itajengwa na wananchi waiamini Serikali yao kwamba yaliyoahidiwa na yaliyoko kwenye Ilani yatatekelezwa. Ahsante sana.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Kwa sasa Barabara ya Tingi – Kipatimu ina maeneo mengi ambayo hayapitiki na mengine yanapitika kwa shida sambamba na Barabara ya Nangurukuru – Liwale.

Je, Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuweza kurekebisha barabara hizo mbili ili ziweze kutengenezwa na hatimaye wananchi waweze kuendelea na shughuli zao za kiuchumi na kijamii?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, barabara hizi mbili za Nangurukuru – Liwale kilometa 258 na hiyo ya Tingi – Kipatimu katika miaka ya karibuni zilipanuliwa upana wake, lile eneo la hifadhi ya barabara kutoka mita 30 hadi kufikia mita 45. Na hii Hali ilisababisha wananchi kuweza kuvunjiwa nyumba zao na kuondolewa mazao yao. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwalipa wananchi ambao hawajalipwa hadi sasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Tingi – Kipatimu ina vilima, na katika swali lake la msingi nimejibu kwamba, tayari TANROADS Mkoa wa Lindi umeainisha maeneo yote korofi ambayo yana vilima na yatawekewa lami. Na hivi tunavyoongea mwaka huu itawekwa walao mita 500 na mwaka wa fedha kama bajeti itapita pia, maeneo yameainishwa ambayo tunategemea kuongeza kiwango cha lami maeneo ambayo barabara inakuwa ina milima na inateleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Barabara ya Nangurukuru – Liwale, yako maeneo ambayo inapita kwenye bonde na maji huwa yanajaa. Na tunategemea kwenye bajeti ya mwaka huu tunayoiendea kama itapitishwa litajengwa tuta kubwa ambapo maji sasa yatakuwa hayana uwezo wa kufurika na kuziba njia hiyo ya Barabara ya Nangurukuru – Liwale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fidia, ni kweli kwamba, baada ya sheria kupitishwa barabara zetu zimetanuliwa kutoka mita 30 hadi 45, lakini 45 hadi 60. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mita hizi ambazo zimeongezeka saba na nusu, sab ana nusu kwa upande, pale ambapo ujenzi utaanza basi wananchi hawa ambao watakuwa ni wathirika watapata fidia wakati mradi huu utakapoanza kutekelezwa kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali iliahidi kwa muda mrefu sana Barabara ya Karatu – Mbulu – Singida na mpaka sasa hamna dalili yoyote ya kujenga kwa kiwango cha lami. Je, ni lini Serikali itatenga hela kwa ajili ya Barabara ya Karatu – Mbulu – Singida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Karatu – Mbulu – Singida ni kati ya barabara ambazo zimeainishwa kwenye ilani na ambazo zinategemea kujengwa kwa kiwango cha lami katika kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Karatu na wananchi wa Karatu na wote watakaonufaika na barabara hizi kwamba, kadiri Serikali itakavyopata hela na katika kipindi hiki cha miaka mitano barabara hizi zitajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali inaendelea kukamilisha ahadi za viongozi waliotangulia. Mheshimiwa wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Jakaya Kikwete alitembelea Wilaya ya Nyan’ghwale na kuahidi ujenzi wa barabara ya lami kutoka Kahama – Nyan’ghwale kwenda Sengerema, lakini mwaka 2015 Hayati Dkt. John Pombe Magufuli naye aliahidi hivyohivyo kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Swali, ni lini Serikali itatenga fedha za upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo la lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye majibu mengine, Barabara ya Kahama
– Nyn’ghwale – Sengerema pale Busisi ni barabara ambazo zimeahidiwa na viongozi wetu na ni barabara muhimu sana kwa kuunganisha maeneo haya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Nyan’ghwale kwamba, barabara hii itafanyiwa upembuzi yakinifu mara bajeti tunayoiendea itakapokuwa imepitishwa. Kwa hiyo, baada ya kufanya hivyo taratibu nyingine kwa maana ya usanifu wa kina utafanyika, ikiwa ni hatua za awali kuelekea ujenzi wa lami wenyewe. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa usanifu ulikamilika na kuwa usanifu unaofanyika ni uhuishaji wa usanifu wa awali. Je, Serikali haioni haja kutenga fedha mwaka ujao wa fedha ili kujenga daraja hilo 2021/2022 ili kunusuru maisha ya wanawake na watoto wanaopoteza maisha kwasababu ya kutokuwa na kivuko hicho?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Kwa kuwa, kivuko kinaanca kazi saa 01:00 asubuhi na kuishia saa 01:00 jioni. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuongeza saa ili kivuko hicho kifikie saa 06:00 usiku kuweza kuwanusuru wananchi wanaopoteza maisha kutokana na saa hizo kuwa fupi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jibu langu la msingi nimeeleza kwamba, tumetenga, kama bajeti itapitishwa kama ilivyoombwa, tumetenga milioni 400 kukamilisha usanifu wa kina.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimueleze Mheshimiwa Mbunge kwamba, daraja hili ni kati ya madaraja makubwa yatakayojengwa Tanzania, Mto Malagarasi ni kati ya mito mikubwa katika Tanzania hivyo, tutakapokamilisha usanifu wa kina ndio ujenzi utaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili ni kivuko kinafanya kazi kuanzia saa 01.00 hadi saa 01.00 jioni.

Mheshimiwa Naibu Spika, naungananae, na kwasababu ya changamoto ya Mto Malagarasi ambao ni mto mkubwa una zaidi ya kilometa 300 na unapita kwenye misitu mikubwa ambayo inabeba magogo na miti, lakini pia kuna wakati unafurika na mpaka zile sehemu zake za ku-park vile viuvuko huwa hazipo ndio maana Serikali imeona isifanye kazi usiku kwasababu, inaweza ikapeleka kivuko ziwani na hata kukipindua hicho kivuko kwa sababu ya hayo magogo na miti.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Mheshimiwa anafahamu kwamba tumeweka utaratibu pale ambapo kuna dharura, watu hao wapo na wamekuwa wanafanya kazi. Hata hivyo, ili kuondokana na changamoto hiyo kabisa ndiyo maana Serikali sasa imekuja na mpango wa kujenga daraja, ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona kwa ajili ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kivuko hiki cha Mto Malagarasi ni muhimu kama ilivyo barabara ya kutoka Kilosa – Magomeni – Masanze -Zombo – Ulaya - Muhenda – Mikumi. Pia barabara hii ilikuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi mwaka 2015-2020 na ipo kwenye Ilani 2020-2025 na ipo kwenye bajeti…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, je ni lini ujenzi wa barabara hii unaenda kuanza? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja imeainishwa kwenye Ilani lakini pia ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Dennis Londo kwamba kuanzia bajeti hii tutakayoianza barabara hii itaanza kufanyiwa kazi kwenye mipango yetu kwani viongozi wengi wameahidi barabara hiyo ijengwe. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi yeye na wananchi wa Mikumi kwamba barabara hii ipo kwenye mpango na itatekelezwa katika kipindi hiki cha miaka mitano.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, naomba nijenge maswali yangu kupitia kwenye hoja tatu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni muhimu sana kwa ajili ya ulinzi wa nchi hii; pia barabara hii ni muhimu sana kwa usafirishaji wa mazao ya ufuta na korosho katika kata zilizopo pembezoni mwa Mkoa wa Mtwara; barabara hii ni muhimu vile vile kwa usafirishaji wa ufuta na korosho kutoka katika maeneo ya nchi jirani ambayo mazao hayo hayana masoko kule:-

(i) Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami? (Makofi)

(ii) Je, Serikali ina commitment gani kwamba barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami na lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela yote mawili kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba tu nitoe taarifa kwamba barabara hii ni barabara ambayo inafunguliwa. Kwa hiyo awamu ya kwanza ni kuifungua barabara hii yenye urefu wa kilometa 365 na ikishafunguliwa ndipo utaratibu wa kuijenga kwa kiwango cha lami utaanza kufanyika.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetambua umuhimu wa barabara hii, kwanza ni barabara ambayo ni muhimu sana kwa vyombo vyetu vya ulinzi na usalama, lakini pia ni barabara muhimu sana kwani ikishafunguliwa itafungua uchumi na itaboresha maisha ya wananchi wengi ambao wanaishi katika kata ambazo amezitaja.

Mheshimiwa Spika, barabara hii inatoka Mtwara hadi Ruvuma na ni barabara ambayo inaambaaambaa na Mto Ruvuma. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya hatua ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha changarawe, hatua za ujenzi kwa kiwango cha lami zitafuata kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuwa barabara hii ni ya muhimu sana kwenye uchumi wa nchi yetu na uchumi wa Kanda wa Ziwa, kwasababu inapunguza umbali wa kutoa Shinyanga mpaka Mkoa wa Mara kuelekea nchi jirani ya Kenya, kwa zaidi ya kilometa 73 na Serikali imekuwa ikiahidi ujenzi wa barabara hii katika Awamu kuanzi ya Tatu mpaka Awamu ya sasa na Wananchi wa Wilaya ya Kwimba wanahitaji kuunganishwa na Makao Makuu yao mkoa wao kwa barabara ya kiwango cha lami.

Je, ni lini sasa Serikali itaachana na maneno ya kutafuta pesa na kuanza kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, barabara inayoanzia Fulo kupitia Nyambiti mpaka Malia yenye urefu wa kilometa 73 pia ni barabara muhimu sana kwenye uchumi wa Wilaya ya Kwimba na barabara hii imeahidiwa kwenye ukurasa wa 77 wa ilani ya Chama cha Mapinduzi kuanza kufanyiwa upembuzi yakinifu na hatimaye kujengwa kwa kiwango cha lami. Je, ni lini sasa Serikali itaanza kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika Awamu ya Tano iliyopita taratibu za ujenzi kwa kiwango cha lami umeanza na ndiyo maana tumekamilisha usanifu wa kina mwaka 2019 kwa hiyo si tu zimekuwa ni ahadi lakini tayari tumeshaanza utekelezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Sumve kwamba barabara aliyoitaja ya Fulo Nyambiti Malia ameisema mwenyewe kuwa imeainishwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi na nimuhakikishie katika kipindi hiki cha Awamu ya Sita kama tulivyosema imeanishwa kwenye ilani, lakini pia imeongelewa na Mheshimiwa Rais wakati analihutubia Bunge hapa ni kati ya barabara ambazo zitafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mbunge na Wananchi wa Sumve kwamba tutatekeleza kama tulivyopanga ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa swali la nyongeza kwa kuwa barabara ya kutoka Kalenga kwenda Ruaha National Park ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa hili hasa unaotokana na utalii na kwa kuwa upembuzi yakinifu na usanifu ulishafanyika siku nyingi. Na kwa kuwa pia Serikali imeweka kwenye ilani tangu Awamu ya Nne mpaka sasa na imekuwa ikitenga fedha kidogo kidogo. Je, kwa nini sasa Serikali isianze kujenga kidogo kidogo kutokana na hizo pesa wanazotenga maana imekuwa ahadi ya muda mrefu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Kiswaga Mbunge wa Kalenga asubiri bajeti tutakayo pitisha nina hakikika ni kati ya barabara kama endapo bajeti itapita itakuwa ni kati ya barabara ambazo zitatekelezwa kuanzia bajeti tunayoiendea. Kwa hiyo, naomba awe na subira na asubiri tutakapo anza kupitia bajeti ya Ujenzi na Uchukuzi.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa majibu ambayo yametolewa kwa kuzingatia kwamba barabara hizi tumezipigia kelele kwa muda mrefu na tunategemea zitusaidie kutuvusha kwenda uchumi wa kati wa juu, kwa sababu ndizo zinakusanya viwanda vyote kule ambapo tunakusanya zaidi bilioni 40 kwa mwaka na pengine kwa miaka kumi ni nusu trilioni. Fedha hizi zote zinakwenda kujenga maeneo mengine, pale wananchi wakitaabika na hivi ninavyozungumza magari hayapatiki.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza la nyongeza; kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri alisema hapa Bungeni mwezi Februari, zingeingizwa kwenye mwaka wa fedha huu 2021/ 2022; na kwa kuwa amezungumza pia usanifu umekamilika wa barabara hii moja. Kwa nini sasa hii iliyokamilika ya kilomita 40 ya kutoka Nyololo mpaka Mtwango isianze kujengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hii ya pili ambayo amesema usanifu unakamilika ni ipi commitment ya Serikali sasa, itaanza lini na itakamilika lini? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini, kwa pamoja, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa amesikiliza jibu la msingi, tunatambua kwamba mbao zote karibu tunazoziona zinatoka eneo la Mafinga zinapita huko, magogo ni mengi. Ndio maana katika jibu langu la msingi nimesema mwaka 2022/2023, Serikali inatoa commitment kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sababu ni barabara ambayo sasa zimekuwa ni changamoto kwetu kutokana na uzito mkubwa kwamba kwa uwezo wa changarawe barabara zinashindwa kuhimili uzito wa magari yanayopita hapo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mufindi Kusini kwamba commitment ya Serikali ni kama tulivyosema kwenye jibu la Msingi tutaanza kujenga 2022/2023. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Barabara ya kutoka Iringa Mjini kwenda Pawaga kilomita 76 ambazo zilikuwa ni ahadi ya hayati Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni mbaya mno na wakulima wa pale wanalima mpunga lakini wanashindwa kusafirisha. Je, ni lini Serikali itakwenda kujenga barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Iringa Pawaga ni kama barabara zingine ambazo zimepata changamoto kubwa katika kipindi hiki cha mvua. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi zipo kwenye ahadi na zitategemea na upatikanaji wa fedha. Pale ambapo fedha zitapatikana barabara hizo zitajengwa na ndioyo azma ya Serikali lakini kinachotukwamisha ni uwezo wa bajeti yetu. Kwa hiyo nimhakikishie fedha zikipatikana barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, Nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tuna Barabara yetu ya Korogwe Mjini ambayo inatokea Old Korogwe, Kwamndolwa, Magoma, Mashewa, Bombo Mtoni mpaka Mabokweni, ambayo ni ahadi ya Marehemu Rais Magufuli, Mama Samia na Waziri Mkuu. Je, ni lini Serikali itatekeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili kutimiza ahadi ya viongozi wetu wa kitaifa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara alizozitaja Mheshimiwa Mbunge wa Korogwe zipo kwenye ahadi ya Rais na zipo kwenye Ilani na ni kati ya barabara ambazo zinakamilisha kilomita 6,006 ambazo zimeahidiwa kujengwa katika kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kadri fedha itakapopatikana barabara hizi ikiwemo na hii zitajengwa kwa awamu. Ahsante.
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali yenye kutia matumaini, nina maswali mawili madogo. Swali la kwanza; kwa kuwa barabara hii inategemewa na wananchi, upande wa Hanang’ tu zaidi ya 100,000 wa Kata za Gisambalang, Bilmaa, Simbai, Isilo, Wareta na Nangwa yenyewe na kulikuwa na Daraja la Mungurwi B. Daraja lile limechukuliwa na mafuriko ya mvua iliyonyesha 2019/2020. Ni kwa nini Serikali daraja lile lilivyochukuliwa halikuwekwa kwenye mpango wa dharura wa kulirudishia?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa daraja lile la Mto Bubu limekuwa likigharimu Maisha ya watu na kupoteza mali kwa kusombwa na maji. Je, Serikali ina mpango gani wa dharulra ili kuhakikisha wananchi wanaendelea na shughuli zao za kijamii pamoja na biashara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samwel Hhayuma, Mbunge wa Hanang’, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba daraja la Mungurwi B lilisombwa na maji na ni daraja ambalo liko sehemu ya bonde ambapo baada ya kusombwa lilitengeneza umbali wa mita zaidi ya 200 na hivyo ilikuwa ni ngumu sana kulijenga kama lilivyokuwa na badala yake, daraja hili linafanyiwa usanifu kutoka ilipokuwa kupanda eneo la juu ambalo tunaamini litakuwa ni eneo fupi, lakini pia hakutakuwa na changamoto ya mafuriko. Kwa hiyo linafanyiwa usanifu na baada ya kukamilika tutaanza kulijenga daraja hilo. Hiyo ndio sababu kubwa ambayo hatukuweka daraja la dharura.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la huo Mto Bubu nadhani nimelijibu pamoja na swali la kwanza kwamba baada ya fedha kupatikana na baada ya usanifu kukamilika, basi hilo daraja litakamilika ili kuunganisha wasafiri kutoka upande wa Kondoa kwenda upande wa Mkoa wa Manyara. Kwa sasa tunawashauri wananchi waendelee kupita kutoka Kondoa kupitia Babati kwenda Katesh na kutoka Sambalang kwenda Babati bila kupita kwenye huo mto. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Swali la msingi linafanana kabisa na Jimbo la Mbulu Vijijini na changamoto iliyopo Hanang’ inafanana kwa sababu ilikuwa ni wilaya moja. Barabara ya kutoka Mugitu kuja Hydom iliahidiwa na ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi na Mheshimiwa Naibu Waziri aliipita. Je, ni lini tunajengewa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatel Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Mugitu - Hydom imeshakamilishwa kufanyiwa usanifu wa kina na sasa hivi kinachosubiriwa ni upatikanaji wa fedha ili ianzwe kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mbulu kwamba kadri fedha zitakapopatikana barabara hii itajengwa pia na ndio maana tayari usanifu wa kina umeshafanyika ikiwa ni maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali iliona umuhimu wa kujenga barabara hii na barabara hii ni ya kimkakati dhidi ya masuala ya kiuchumi ambayo inakwenda kujengwa kwa ajili ya kuinua uchumi wa Kikanda, Kimkoa na Kitaifa, na barabara hii ilishafanyiwa upembuzi wa kina na upembuzi huo ulishakamilika toka mwaka 2018. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kupeleka huko kwa ajili ya kuana ujenzi huo haraka iwezekanavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ucheleweshaji wa ujenzi wa barabara hii ya kimkakati ambao unachukua muda mrefu sana kuanza kujengwa je, Serikali haioni kwamba kutokuanza kujenga barabara hii kwa haraka inaendelea kusababisha udumavu wa ukuaji wa uchumi katika Mkoa wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina urefu wa kilometa 521 kwa hiyo ni uwekezaji mkubwa na tayari tulishaanza jitihada za kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kwa hatua za awali ikiwa ni pamoja na hizo hatua ambazo tayari zimeshafanyika usanifu wa kina lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Msongozi kwamba tayari tumeshaanza ujenzi wa kiwango cha lami katika vipande kadhaa ambavyo nimevitaja ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwango cha lami kilometa 66.9 kuanzia Kidatu kwenda Ifakara, na bado tumehakikisha kwamba barabara hii itakwenda kutengenezwa kadri fedha zitakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nia ya Serikali ni kuikamilisha barabara hii ili kuifungua Ruvuma na kanda yote ya kusini ambayo inatumia barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kadri fedha zitakapoendelea kupatikana barabara hii tutahakikisha tunaiunganisha kwa Mikoa ya Ruvuma na Morogoro kupitia kwenye hiyo barabara ambayo amesema ambayo inapita kwenye mbuga za Selous na ni miinuko mikali kwa hiyo, uwekezaji ni mkubwa lakini Serikali inatafuta fedha na tunahakikisha tutaijenga, ahsante.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali, swali langu ni kwamba mwezi mmoja uliopita daraja lilikatika katika mji wetu wa Tarime na likasababisha vifo vya watu watatu na wengine watatu mpaka sasa hivi hawapatikani na inadhaniwa kwamba walikwenda na maji, na hata sasa hivi ninavyozungumza kuna daraja limekatika kipande kimoja daraja ambalo linatoka mjini kuelekeza Kibaga ambako wanachimba madini na kuna magari makubwa yanabeba makinikia yanapita pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba je, ni lini watarekebisha hili daraja ili lisije likaleta maafa mengine kama ilivyosababishwa na kuvunjika kwa daraja, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba Serikali inatambua kwamba mwaka huu kumekuwa na uharibifu mkubwa sana wa barabara nyingi na hasa hizi za changarawe na udongo. Na sisi kama Wizara tulishalitambua hilo tuna maandalizi ambayo tulishayafanya ikiwa ni pamoja na kununua madaraja ya dharula lakini imekuwa ni vigumu sasa hivi kutengeneza hizo barabara kwasababu nyingi sio tu zinahitaji kuweka madaraja lakini pia zinahitaji kuweka matuta ambayo yanainuliwa sasa inakuwa ni ngumu kufanya kazi hiyo katika kipindi hiki ambacho mvua inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wengine kwamba barabara zote inaainishwa zile ambazo zimepata changamoto hasa kutokana na mvua na mara hali ya hewa itakapokuwa vizuri wakandarasi wapo tayari watazirejesha barabara hizi zote katika hali yake ya kawaida ili ziendelee kutumika ikiwa ni pamoja na barabara ya Mheshimiwa Michael Kembaki Mbunge wa Tarime.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kuniona hali ya barabara ya Lumecha kilosa inafanana kabisa na ile ya Bungwi Nyamisati je, ni lini sasa Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami ikizingatiwa ni muhimu kwa wananchi wa Mafia, Mkuranga na Kibiti yenyewe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri barabara ya Bungwi Nyamisati nimefika na tukiwa tumeongozana na Mheshimiwa Mbunge Mpembenwe naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba hii ni barabara ambayo ni ahadi ya viongozi wa Kitaifa lakini pia ipo kwenye Ilani ambayo inaunganisha wananchi wa Mafia na wanaokuja bara, kwa hiyo ipo kwenye mpango, fedha itakapopatikana barabara hii itajengwa ili kuifanya wananchi waweze kupata huduma bora ya barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali iliahidi babarara ya Njiapanda Mang’ola, Matala Mwausi Lalago, kwa kiwango cha lami kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi sasa ni lini bararara hiyo itajengwa kwa kiwango cha Lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, tunategemea kupitisha ama kuleta bajeti yetu ili iweze kujadiliwa naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira ili kipindi cha bajeti tutaitolea maelezo sahihi kuhusu hiyo barabara ambayo ameisema na nimhakikishie tu kama nilivyosema kwenye majibu mengine ya msingi na wananchi wa Jimbo lake kwamba barabara ambazo zote zimeahidiwa na kuwa kwenye Ilani zipo kwenye mpango wa Kipindi cha Miaka Mitano na tutazijenga kadri ya fedha zitakapoendelea kupatikana. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa barabara ya Loliondo – Wasu - Mto wa Mbu ni ahadi ya muda mrefu kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami. Natambua kuna kipande cha Waso - Sale kilometa 49 sasa hivi kinaendelea kujengwa kwa kiwango cha lami ila kuna eneo korofi sana la Sale – Ngaraesero, je, ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupitia Bunge lako nimuagize Meneja wa TANROADS Mkoa aweze kwenda kwenye barabara hii ya Sale - Ngaraesero ili aweze kufanya tathmini na aone kama tunaweza tukajenga kipande; imekuwa ni kawaida sehemu ambayo tunaona ni korofi yenye vilima ama yenye miteremko mikali ama yenye utelezi aende akafanye tathmini na kuleta bajeti ili tuone namna ambavyo tunaweza tukafanya ili tusikwamishe wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba Mheshimiwa awe na amani na ikiwezekana baada ya kikao hiki tuweze kukutana ili aweze kunipa taarifa kamili ya eneo hilo ili tuweze kulifanyia kazi. Ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Wizara. Hii barabara ni muhimu sana kwa upande wa Rungwe lakini pia kwa upande wa Ileje. Ni barabara kwa upande wa Rungwe inapita kwenye Kata ya Kyimo, Iponjola pamoja na Ikuti ambapo kuna milima mikali, barabara muda mwingi inakuwa sio nzuri. Kwa hiyo naomba Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ituambie exactly ni lini hii barabara itaanza kufanyiwa upembuzi yakinifu ili ijengwe kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni lini barabara ambayo pia ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2020 - 2025 kutoka Kiwira kupitia Kata ya Kinyala, Igogwe mpaka Mbalizi itafanyiwa pia upembuzi yakinifu na kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Anton Mwantona, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Ibungu –Kalembo – Katengele - Sange - Luswisi – Kafwafwa - Ikuti hadi King’o ni kweli ni barabara ambayo ni muhimu sana kwa wananchi wa Ileje na Rungwe. Nataka nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutahakikisha kwamba katika awamu hii ya miaka mitano barabara hii inafanyiwa usanifu na upembuzi yakinifu na mimi ni mnufaika kwa sababu inapita kwenye Jimbo langu na kwenye Kijiji changu pia cha Kalembo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mbunge kwamba barabara hii itafanyika kama tulivyoahidi kwenye Ilani ya Uchaguzi. Pia, barabara hii ya Kiwira – Kinyala - Igogwe hadi Mbalizi nayo pia iko kwenye Ilani ambayo nayo pia imeainishwa kati ya barabara zile ambazo zitafanyiwa usanifu wa kina. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Rungwe na wa Ileje kwamba barabara hizi tutahakikisha kwamba zinafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi ya ujenzi wa lami kadri fedha zitakavyopatikana. Ahsante.
MHE. MOHAMED M. LUJUO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa muda ili niulize swali langu la nyongeza. Barabara inayounganisha Wilaya ya Kiteto na Makao Makuu ya Mkoa wao wa Manyara inapita kwenye Jimbo langu, lakini sehemu ya barabara hiyo Kijiji cha Kelema Maziwani daraja limekatika na ni miezi sita sasa. Sasa, naomba kujua ni lini daraja hili litajengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Moni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, TANROADS wanafanya tathmini ya barabara zote ambazo zimepata changamoto ya mvua ikiwa ni pamoja na madaraja. Wizara kupitia TANROADS kutokana na uzoefu uliotokea miaka miwili, mitatu iliyopita tumeandaa madaraja ya muda kwa ajili ya kutatua changamoto za madaraja ambayo yamesombwa ama kuharibika. Sasa hivi inakuwa ni ngumu kurekebisha hayo madaraja kwa sababu yanahitaji kutengeneza tuta halafu madaraja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hata ungeweka sasa hivi ni wazi kwamba daraja hilo litasombwa kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba daraja hilo ambalo liko katika hiyo barabara ya Kiteto Manyara litakuwa ni kati ya madaraja ambayo yatahakikishwa kwamba yanajengwa ili kurudisha mawasiliano ambayo yamekatika kwa kipindi alichokitaja Mbunge. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja la nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kipande cha barabara ya kutoka Uvinza hadi Malagarasi, kilometa 48, Serikali iliahidi kukijenga kwa msaada wa pesa za Falme za Kiarabu. Tangu mwaka juzi, 2019 Serikali imekuwa ikisema kwamba kipande hicho kitajengwa kwa pesa hizo za msaada wa Falme za Kiarabu:-

Je, ni lini sasa Serikali itajenga kipande hicho cha kutoka Uvinza hadi Malagarasi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Malagarasi hadi Uvinza yenye urefu wa takribani kilometa 53 ni kati ya barabara kuu ambayo inaunganisha Mkoa wa Kigoma na Tabora. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo fedha ipo na muda wowote, hata kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha huu, itatangazwa kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami ili sasa tuweze kukamilisha barabara kwa kiwango cha lami kutoka Kigoma – Malagarasi – Kaliuwa – Urambo – Tabora hadi Dodoma. Ahsante sana.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Halmashauri ya Mji wa Bunda ni makutano kati ya barabara itokayo Ukerewe – Mwanza – Simiyu kwenda Sirari – Tarime – Musoma kuja Mwanza na Serengeti kuja Mwanza:-

Je, ni lini Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi itaweka taa za barabarani za kuongoza magari ili kupunguza ajali zinazotokea eneo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba, kwa sasa barabara zote zinazojengwa na zinazopita kwenye miji, katika mikataba lazima watengeneze barabara katika miji. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, mpango upo sasa wa TANROADS kuhakikisha kwamba sehemu zote za miji ambazo zilikuwa hazina barabara za kuongozea magari kama alivyosema, wafanye usanifu ili tupate gharama yake na tuweze kuweka taa za kuongozea magari, hasa maeneo ambayo yana magari mengi. Kwa hiyo, study hiyo inaendelea. Naamini Bunda itakuwa ni sehemu ya wanufaika. Ahsante.
MHE. ANTHONY P. MAVUNDE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ubovu wa Barabara ya Ihumwa – Hombolo unaleta adha kubwa kwa wananchi wa Chahwa, Ipala na Hombolo yenyewe na hivyo kuongeza gharama za usafiri: Je, ni lini sasa Serikali itakuwa tayari kutekeleza mpango wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Ihumwa mpaka Hombolo ili kuwaondolea adha wananchi hawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni azma ya Serikali kujenga barabara zote kwa kiwango cha lami, lakini suala hili linafanyika kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Barabara ya Ihumwa – Hombolo hadi Mayamaya yenye urefu wa takribani kama kilometa 7.3 ni ya kiwango cha changarawe na kama fedha itapatikana, itajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba muda wote inapitika ili wananchi wa eneo hilo ikiwa ni pamoja na wanafunzi na wafanyakazi wa Chuo cha Hombolo wasiweze kupata taabu. Kwa hiyo, tumetenga fedha kwa matengenezo ya muda na kuhakikisha kwamba maeneo yote yale korofi yanatengenezwa ili kusiwe na changamoto ya usafiri na usafirishaji kwa barabara hiyo. Ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, swali la kwanza, ni jepesi tu; ni lini ujenzi unaanza, basi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kama Serikali ya Ujerumani imeweza kutoa fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu, inakuwaje Serikali inasuasua kutoa fedha kwa ajili ya usanifu wa kina? Hivi hata hao wanatoa fedha za ufadhili katika hatua hizi za awali hatuoni kama tunawa-discourage kwa kitendo cha Serikali kusuasua kutoa fedha za kuendeleza mradi huu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni hayo tu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Nyongo, Mbunge wa Maswa Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu la msingi nimesema barabara hii itaanza mara fedha itakapopatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimhakikishie katika swali lake la pili, kuhusu kwamba Serikali inasuasua. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi hii Barabara inapita Maswa – Lalago – Mwanhuzi – Sibiti – Hydom – Mbulu – Karatu. Katika baadhi ya barabara, hii tayari kama mlivyosikia jana kwenye bajeti, kipande cha Mbulu – Haidom kitaanza kujengwa. Pia Mheshimiwa Waziri jana amesema barabara hii itatangazwa siku za karibuni ambayo ni sehemu ya hii barabara kwa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, hata hicho kipande ambacho sasa tutafanya ni design and build, yaani ni kufanya usanifu na ujenzi, basi hela ikipatikana hata kipande hiki cha Lalago – Maswa kitajengwa. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Changamoto zilizoko Maswa Mashariki kuhusu barabara zinafanana sana na changamoto ambazo ziko Arumeru Mashariki. Kuna barabara inayoanzia Tengeru kwenda Mererani, inaunganisha Mkoa wa Arusha na Manyara, lakini pia ni kiungo muhimu kwa shughuli za uchimbaji Mererani na soko ambalo liko Mjini Arusha. Je, ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara hii ni muhimu sana na Mheshimiwa Pallangyo amekuwa akiifuatilia sana, lakini bado tunasema nia ya Serikali ni kujenga hizi barabara ambazo zimeainishwa na zinarahisisha maisha ya wananchi kama zitajengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Pallangyo, Serikali inaendelea kutafuta fedha na fedha ikipatikana basi hii Barabara ya Tengeru kwenda Mererani, sehemu ambayo kuna machimbo ya tanzanite itajengwa ili kuweza kuboresha maisha na kupandisha uchumi, lakini pia kurahisisha biashara ya tanzanite kule Arusha. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza ambayo ningependa kupata majibu yake. Swali la kwanza; kwa kuwa barabara hii ni kiunganishi muhimu ambacho kinaunga Chato na Biharamulo kuelekea katika Hifadhi ya Taifa ya Burigi Chato, ningependa kujua sasa kwamba construction period ya barabara hii itakuwa ni miezi mingapi ili nijue na wananchi wale waweze kujipanga kwa ajili ya kuchukua fursa za pale?

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuzingatia umuhimu wa Hifadhi ya Chato Burigi na location ya Uwanja wa Ndege wa Geita Chato ulipo, sasa ningependa kujua je, Serikali haioni ni wakati muhimu sasa wa kuijenga barabara hii sambamba na barabara ya Mkingo – Chato kupitia Kaswezibakaya ili iweze kuunganisha Kabindi pale watu wanaokuja waweze kutoka vizuri? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi ni kwamba barabara hii imetengewa fedha kwenye bajeti hii na yeye Mheshimiwa Mbunge ni shahidi. Kipindi cha matengenezo kitategemea na hali halisi, lakini cha msingi tu ni kwamba mara bajeti itakapoanza barabara hii itaanza kujengwa, lakini kipindi kitakachotumika itategemea na taratibu za manunuzi zitakavyokamilika, lakini pia na hali ya hewa itakayokuwepo. Kwa hiyo, ni ngumu kusema itachukua muda gani, lakini tutaanza kujenga mara tu bajeti itakavyoanza kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, barabara hii itaendelea kukarabatiwa katika kiwango cha changarawe. Hata hivyo, azma ya Serikali ni kuijenga kwa kiwango cha lami kadri fedha itakavyopatikana ili watalii na watu mbalimbali waweze kupita kwenye hizo mbuga za wanyama na kufika kwenye Uwanja wa Ndege wa Chato. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante; pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kutokana na umuhimu wa barabara ya ulinzi inayozunguka maeneo ya mipaka yet una nchi Jirani ya Msumbiji, je, lini Serikali itaanza kutengeneza barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili kurahisisha hata vyombo vyetu vya ulinzi vinapofanya doria vifike kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kutokana na uwepo wa miundombinu muhimu ya umeme na visima vya gesi, Vijiji vya Msimbati na Madimba. Je, Serikali haioni sasa ni wakati sahihi wa kuboresha miundombinu ya barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shamsia Azizi Mtamba, Mbunge wa Mtwara Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya ulinzi aliyoitaja ni barabara muhimu sana na ina urefu zaidi ya kilometa 350 na hadi sasa barabara hii baada ya kwamba ilitumika kipindi kile haitumiki na sasa hivi inafunguliwa upya na tayari na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) imeshafungua karibu kilometa 250 na inaendelea kuifungua mpaka itakapokamilika. Na baada ya kukamilika kuifungua ndipo tutakapoanza utaratibu wa kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, barabara hii aliyoisema ni lini tutaanza, tayari tumeshaanza ndio maana tumeshafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kilichobaki sasa ni kutafuta tu fedha na tutakapopata basi tutaanza kujenga kwa kiwango cha lami ili kufikia hayo maeneo muhimu ya Mnazi Bay, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; ni barabara nyingi sna Tanzania hii unakuta zimeharibika na zinasababisha ajali. Nilitaka kujua mpango mkakati maana yake Waziri amekiri kwamba ni kwa sababu ya malori yenye mizigo mizito yanapita yanasababisha uharibifu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami ambayo itastahimili haya malori ambayo yanakuwa yanapita na mizigo mikubwa na kuharibu barabara na hivyo kusababisha ajali nyingi na kupoteza maisha ya watu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu Serikali ina project ambayo inaendelea ya SGR na vitu vingine. Ni lini itakamilika sasa ili mizigo mingi iweze kusafirishwa kwa njia ya reli na siyo kutegemea barabara ili barabara ziweze kutumika kwa usafiri wa mabasi na magari mengine madogo madogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Kwanza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati wote tunapofanya design ya barabara tunategemea na kiasi cha mizigo itakayopita na ukubwa wa barabara. Lakini kwa sababu ya mabadiliko ya uchumi kumekuwa na mabadiliko makubwa sana ya uchumi ambayo yanapelekea magari ambayo yalikuwa yamepangiwa kupita barabara hiyo hayabadiliki na hivyo lazima tubadilishe design na ndiyo maana tunafanya matengenezo na tunapofanya matengenezo kwenye barabara hizi tunahakikisha tunapofanya matengenezo ambayo sasa magari makubwa na mazito yatapita kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mkakati wa Serikali ni kufanya rehabilitation kubwa kwenye hizi barabara ambazo tunaamini zitachukua magari makubwa na yenye mizigo mizito.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imekuwa ikisimamia na imeendelea kutoa fedha na ni mpango wa Serikali kuanzisha ujenzi wa SGR ili kunusuru barabara zetu na kuhakikisha kwamba mizigo mikubwa sasa badala ya kupita kwenye barabara ipite kwenye reli ya kisasa ambayo SGR na ndiyo maana tayari sasa barabara inaendelea kujengwa na fedha zinaendelea kutolewa ili kupunguza mizigo mikubwa itakayopita kwenye barabara zetu na kunusuru hizo barabara, ahsante.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kusini ile tunayoita ya Kilwa-Mtwara nilizungumzia hapa ni barabara mbovu kuliko barabara nyingine zote. Sambamba na hilo tunawashukuru Serikali kwa kututengea hizo pesa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo. (Makofi)

Sasa swali langu ni kwamba Serikali imesema imetoa ushauri tusafirishe hiyo mizigo kwa njia ya bandari; je, meli ya mizigo kwa ajili ya kusafirisha hiyo cement iko tayari au lini itakuwa tayari?
NAIBU WAZIRI UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali ni kuboresha usafirishaji na ndiyo maana Bandari ya Mtwara imepanuliwa ili iweze tu si kusafirisha mizigo mikubwa lakini pia kufungua Mikoa ya Kusini.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti na tumesema tutakuwa na ujenzi wa meli kubwa itakayokuwa inafanya pwani ya Bahari ya Hindi, lakini nilichosema kwenye jibu langu la msingi, ni kuwahamasisha wafanyabiashara wa ndani na wa nje sasa kutumia bandari yetu, kutumia meli mbalimbali za kibiashara ambapo bandari hii ya Mtwara ina uwezo wa kupokea meli kubwa na uwezo wa kushusha shehena kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge na wale ambao wanafanyabiashara; kupitia Bunge lako napenda kuwataarifu kuwa Bandari ya Mtwara sasa iko tayari kupokea mizigo mbalimbali kwa ajili ya kusafirisha hiyo mizigo na kupunguzia uzito barabara yetu ambayo sasa inaharibika mara kwa mara, ahsante. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante na nashukuru sana kwa majibu ya Waziri, lakini sasa napenda nijue ni lini zoezi hili litaanza la ujenzi wa hiyo barabara? Naomba kupatiwa majibu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Minza Mjika kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nimeainisha kwamba tayari tumeshaanza ujenzi kwenye baadhi ya maeneo na katika bajeti tutakayoanza kuitekeleza ambayo Bunge lako limepitisha, tumetenga fedha, kwa hiyo, mara tu bajeti itakapoanza kutumika barabara hiyo itaanza kujengwa, ahsante.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali ilianza ujenzi wa barabara ya lami inayotoka Sanya Juu kwenda Kamwanga ambapo ingeungana na nyingine inayotoka Rombo kuja mpaka Kamwanga na barabara hii imesimama ujenzi wake pale Kijiji cha Elerai wakati zimebaki zimebaki kilometa 42.8 tu kukamilika.

Naomba kufahamu Serikali itaendeleza lini ujenzi wa barabara hii ambayo sasa ni mwaka wa pili tangu isimame?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Kiruswa, Mbunge wa Longido kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kati ya barabara ambazo zimeainishwa kwenye bajeti yetu na kama tulivyoahidi kwenye bajeti zetu tuna uhakika bajeti itakavyoanza kutekelezwa basi itaendelea kutekelezwa kama tulivyoahidi kwenye bajeti yetu ambayo imepitishwa, ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, wananchi wa Jimbo la Mlimba ukiwauliza tatizo lao kubwa ni barabara unaweza kuacha yote lakini barabara ni kipaumbele cha kwanza.

Naomba niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo kwa niaba ya wananchi wa Mlimba; ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi rasmi wa barabara ya kiwango cha lami kutoka Ifakara - Ng’ambo - Mto Lumemo mpaka Lupembe Madeke yenye urefu wa kilometa 223? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Kunambi, Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ambayo ambayo ameitaja inayoanzia Mikumi, Ifakara, Mlimba, Madeke hadi Lupembe na hadi Kibena Junction ni barabara inayounganisha mikoa miwili na imetengewa fedha kwenye bajeti ambayo itaanza kutekelezwa kuanzia upande wa Njombe na kuanzia upande wa Jimbo lake kwenye sehemu mbili.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mara bajeti itakapoanza kutumika kama tulivyoahidi kwenye bajeti barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa barabara ya kutoka Bariadi - Itirima - Mwandoya mpaka Isibiti Iguguno ni kilometa 289 na iko kwenye Ilani. Je, ni lini Serikali itaanza kuijenga kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara anayoisema inatoka Mwandoya junction kwenda Mwandoya ni barabara ambayo ilikuwa bado haijafanyiwa usanifu wala upembuzi yakinifu.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha huu barabara hii imepangwa kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili iwe sasa tayari kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, nikisikia barabara inayotoka Simiyu kuja Kolandoto ni kama inanitonesha vile kidonda. Mheshimiwa Naibu Waziri ulisema tender itatangazwa; je, lini mnatangaza tender kwa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara anayoisema ya Mbulu na hasa Mbulu Hydom yenye kilometa 50 ipo kwenye mpango wa kutangazwa kabla ya mwisho wa bajeti ya mwaka huu. Kwa hiyo, taratibu zote za manunuzi zote zinakamilisha, muda wowote barabara hii itatangazwa kabla ya kuanza bajeti ya mwakani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ambayo pia Mheshimiwa aliombea kupiga sarakati itatangazwa kabla ya mwisho wa mwaka huu, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; ni barabara nyingi sna Tanzania hii unakuta zimeharibika na zinasababisha ajali. Nilitaka kujua mpango mkakati maana yake Waziri amekiri kwamba ni kwa sababu ya malori yenye mizigo mizito yanapita yanasababisha uharibifu wa barabara.

Mheshimiwa Spika, mpango mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami ambayo itastahimili haya malori ambayo yanakuwa yanapita na mizigo mikubwa na kuharibu barabara na hivyo kusababisha ajali nyingi na kupoteza maisha ya watu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu Serikali ina project ambayo inaendelea ya SGR na vitu vingine. Ni lini itakamilika sasa ili mizigo mingi iweze kusafirishwa kwa njia ya reli na siyo kutegemea barabara ili barabara ziweze kutumika kwa usafiri wa mabasi na magari mengine madogo madogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Kwanza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati wote tunapofanya design ya barabara tunategemea na kiasi cha mizigo itakayopita na ukubwa wa barabara. Lakini kwa sababu ya mabadiliko ya uchumi kumekuwa na mabadiliko makubwa sana ya uchumi ambayo yanapelekea magari ambayo yalikuwa yamepangiwa kupita barabara hiyo hayabadiliki na hivyo lazima tubadilishe design na ndiyo maana tunafanya matengenezo na tunapofanya matengenezo kwenye barabara hizi tunahakikisha tunapofanya matengenezo ambayo sasa magari makubwa na mazito yatapita kwenye barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mkakati wa Serikali ni kufanya rehabilitation kubwa kwenye hizi barabara ambazo tunaamini zitachukua magari makubwa na yenye mizigo mizito.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imekuwa ikisimamia na imeendelea kutoa fedha na ni mpango wa Serikali kuanzisha ujenzi wa SGR ili kunusuru barabara zetu na kuhakikisha kwamba mizigo mikubwa sasa badala ya kupita kwenye barabara ipite kwenye reli ya kisasa ambayo SGR na ndiyo maana tayari sasa barabara inaendelea kujengwa na fedha zinaendelea kutolewa ili kupunguza mizigo mikubwa itakayopita kwenye barabara zetu na kunusuru hizo barabara, ahsante.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kusini ile tunayoita ya Kilwa-Mtwara nilizungumzia hapa ni barabara mbovu kuliko barabara nyingine zote. Sambamba na hilo tunawashukuru Serikali kwa kututengea hizo pesa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo. (Makofi)

Sasa swali langu ni kwamba Serikali imesema imetoa ushauri tusafirishe hiyo mizigo kwa njia ya bandari; je, meli ya mizigo kwa ajili ya kusafirisha hiyo cement iko tayari au lini itakuwa tayari?
NAIBU WAZIRI UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali ni kuboresha usafirishaji na ndiyo maana Bandari ya Mtwara imepanuliwa ili iweze tu si kusafirisha mizigo mikubwa lakini pia kufungua Mikoa ya Kusini.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti na tumesema tutakuwa na ujenzi wa meli kubwa itakayokuwa inafanya pwani ya Bahari ya Hindi, lakini nilichosema kwenye jibu langu la msingi, ni kuwahamasisha wafanyabiashara wa ndani na wa nje sasa kutumia bandari yetu, kutumia meli mbalimbali za kibiashara ambapo bandari hii ya Mtwara ina uwezo wa kupokea meli kubwa na uwezo wa kushusha shehena kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge na wale ambao wanafanyabiashara; kupitia Bunge lako napenda kuwataarifu kuwa Bandari ya Mtwara sasa iko tayari kupokea mizigo mbalimbali kwa ajili ya kusafirisha hiyo mizigo na kupunguzia uzito barabara yetu ambayo sasa inaharibika mara kwa mara, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na nashukuru kwa ujenzi unaofanyika. Licha hivyo nina maswali mawili mafupi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, tukiwa tunasubiri upatikanaji wa fedha na kwa kuwa upembuzi yakinifu umefanyika kwa muda mrefu, je, kuna mkakati gani wa Serikali wa muda mfupi wa ukarabati na kutambua sehemu korofi za barabara hii ya Mikumi – Kilosa ambao unaweza ukafanyika kwa upande wa lami nyepesi kwenye sehemu korofi?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa barabara hii inaendelea mpaka Magore, Tuliani, Mziha, Handeni kule Tanga; na sehemu ya Tuliani mpaka Mziha bado haijajengwa kwa kiwango lami. Ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami ili barabara hii ikamilike? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Ishengoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara kipande cha kuanzia Kilosa mpaka Mikumi fedha ya matengenezo ipo.

Kwa kuwa mvua ilikuwa inanyesha baada ya mvua tu kukatika wakandarasi watakwenda kazini kuhakikisha kwamba maeneo yote yale ambayo yalikuwa yana tatizo yanarekebishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu kuweka lami nyepesi itakuwa ni gharama kwa sababu barabara hiyo iko kwenye mpango wa matangenezo na fedha inapopatikana tunaendelea kuijenga. Tutakachofanya tu ni kuikarabati kwa kiwango cha changarawe ili iendelee kupitika lakini tutakapopata fedha tutajenga barabara zote kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu barabara ya kuanzia Mziha – Turiani, katika bajeti ya mwaka huu fedha imetengwa kwa ajili ya kuendelea kuanzia Turiani na kuendelea upande wa kwenda Tanga. Kwa hiyo, kama ataangalia bajeti iliyopitishwa fedha imetengwa kwa barabara zote hizo mbili kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara hii swali lilkuwa ni lini ujenzi utaanza. Lakini barabara hii haina tofauti na barabara nyingine ya kutoka Kilosa kuja Mikumi ambayo ipo kwenye Ilani ya mwaka 2015/2020, 2020/2025 na ipo kwenye bajeti hii ya mwaka huu na bado tunaambiwa kwama ipo kwenye maandalizi. Sasa Je, ni lini ujenzi wa barabara hii unaenda kuanza? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nniaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Londo, Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti ni kweli barabara ile aliyotaja ya Kilosa Mikumi ipo kwenye Ilani na imetengewa fedha kwa bajeti inayokuja. Kwa hiyo, tunaamini kwamba tutakapoanza utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2021/2022 basi hii barabara itakuwa moja ya barabara ambazo zitaendelea kujengwa kwani tayari barabara hii upande inapoanzia eneo la hapa njia panda barabara ya Morogoro – Dodoma; tayari imeshajengwa mpaka Kilosa na tunaendelea na ujenzi. Kwa hiyo kipande kilichobaki cha Kilosa kwenda Mikumi barabara hii naamini nayo itaanza kujengwa katika bajeti tunayoanza kuitekeleza. Ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, umuhimu wa barabara hii inayotajwa pia upo kwenye kufungua Mkoa wa Lindi na kwa ajili ya uchumi wa Kusini. Lakini Serikali mara nyingi imekuwa ikiongea tu kuhusu eneo hili la kusahau junction inayoanzia maeneo ya Mbingu kule Ifakara inapita Liwale inakwenda kutokea Nachingwea mpaka Masasi na yenyewe ni muhimu kama ilivyo hivyo.

Sasa Serikali itueleza hapa kwa sababu tulikuwa tukiongea kuhusu barabara hii mara nyingi kwamba ni lini sasa pamoja na nia njema ya kutaka kutengeneza hii barabara inayokwenda Ruvuma mtamalizia na ile junction inayokuja kutokea Liwale kuja Nachingwea mpaka Lindi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwambe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja kuanzia Mbingu, Liwale hadi Nachingwea ni barabara ambayo kweli ipo imeahidiwa lakini ujenzi wa barabara hii utategemea na upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, kwanza itatakiwa ifanyiwe upembuzi na baadaye usanifu wa kina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumepitisha bajeti, kwa hiyo, itategemea na upatikanaji wa fedha ambayo kama itapatikana fedha basi miradi hii itaanza kutekelezwa sawasawa na miradi mingine. Lakini kikubwa ni ufinyu wa bajeti ambao unafanya barabara hizi zote haziwezi kutekelezwa kwa wakati mmoja. Lakini ni nia ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa ili kuweza kufungua maeneo haya na pia kupunguza umbali ambao wananchi wanasafiri kuzungukia barabara ambazo ni ndefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri ambayo yanaonesha kwamba kwa kweli Serikali inafanya kazi nzuri sana, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, je, fedha ambazo kiasi kilichotengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo shilingi bilioni 2.5 zinatosha kukamilisha barabara hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Jimbo la Arumeru Magharibi mazingira yake kwa maana ya miundombinu sio mizuri kabisa. Naomba kujua je, tuna barabara mbili, barabara ya Malalua – Nduruma – Bwawani inayounganisha Simanjiro na Arumeru Magharibi na barabara ya TPRA – Likamba inayounganisha na Monduli.

Je, haioni sasa ni busara kwa ajili ya mazingira ya Jimbo hilo magumu barabara hizo mbili kupandishwa hadhi kupelekwa TANROADS? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba fedha iliyotengwa haiwezi ikakamilisha kilometa 18, lakini hii ni fedha ya awali kwa ajili ya kuanza mradi na wakati huo Serikali itaendelea kutafuta fedha ili kukamilisha mradi huu. Mradi huu utaenda kwa awamu, fedha iliyopatikana tutaanza na kazi na kazi itakavyozidi kupatikana basi tutakamilisha huu mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili nimshauri Mheshimiwa Noah Lemburis, Mbunge wa Arumeru Magharibi kwamba hizo barabara ambazo amezitaja kuna utaratibu maalum ambao kama barabara inatakiwa ipandishwe hadhi zipo taratibu, ziko kanuni ambazo zinapitia kwenye vyombo kuanzia Halmashauri kwenda kwenye DCC, kwenda Mfuko wa Barabara wa Mkoa hadi RCC ambao wanaleta hayo maombi kwenye Wizara yetu na sisi tunafanya tathmini na kuona inakidhi vigezo vya kupandishwa daraja ili barabara hizo ziweze kuhudumiwa na Wakala wa Barabara TANROADS. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Noah uende ukafanya mchakato huo nasi tutafanya tathmini na kama zitakidhi vigezo barabara hizo zitasimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Kwa kuwa Mkoa wa Morogoro ni Mkoa pekee nchini ambao haujaunganishwa kwa kiwango cha lami na mikoa mitatu; Mkoa wa Lindi, Mkoa wa Ruvuma, na Mkoa wa Njombe.

Sasa swali langu dogo la nyongeza ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami yenye kilometa 223 kutoka Ifakara – Mlimba mpaka Madeke -Lupembe – Njombe? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Kunambi kwa kufuatilia hiyo barabara. Mikoa aliyoitaja ni kweli barabara hazijaunganishwa kwa kiwango cha lami, lakini barabara zipo japo zinapitika kwa shida sana.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kunambi kwamba katika bajeti tunayoanza kuitekeleza atakubaliana nami kwamba Serikali imetenga fedha kuanza ujenzi wa barabara hiyo ya kuanzia Ifakara – Mlimba – Madeke mpaka Kibena Junction kwa kiwango cha lami.

Kwa hiyo, kwenye bajeti tunayoanza kuitekeleza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kunambi na wapiga kura wa Jimbo la Mlimba kwamba Serikali imejipanga utekelezaji kwa kiwango cha lami wa barabara hiyo utaanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa daraj ala Godegode linalounganisha majimbo mawili yaliyoko katika Wilaya ya Mpwapwa lilichukuliwa na maji msimu wa mvua wa mwaka 2020 na kusema ukweli uchumi wa wananchi wa Majimbo haya mawili, Jimbo la Kibakwe na Jimbo la Mpwapwa yanategemea sana uwezo wa daraja hili, lakini pia tukizingatia kwamba daraja hili ujenzi wake uko kwenye Ilani ya Uchaguzi 2020/2025.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa daraja hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Malima Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nimuombe Mheshimiwa Malima baada ya session hii tuweze kuonana ili kama daraja limeondoka, kujenga daraja inaweza ikachukua muda, lakini tuna madaraja ya chuma ambayo yanaweza yakatumika kwa muda wakati Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kujenga hilo daraja kwa muda mrefu. Lakini kwa maana inaunganisha Halmashauri au Wilaya mbili nadhani itakuwa ni busara tuonane nae ili tuone na wataalam kupitia Bunge hili Mkoa huu wa Dodoma basi waende wakafanye tathmini ili tuweze kuona kama tunaweza tukajenga daraja la muda wakati tunatafuta fedha ya kujenga daraja la kudumu ili shughuli za uchumi na usafirishaji na usafiri wa wananchi ziweze kufanyika katika kipindi cha muda mfupi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona na naomba nitumie fursa hii pia kukupongeza kwa Kiti hicho ulichokikalia, kwa kweli umekitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu dogo la nyongeza linahusu ahadi ya muda mrefu sana ya barabara ya lami ambayo iliahidiwa itoke Longido mpaka Siha kuunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Kilimanjaro kutokea Longido ambayo iko kwenye Ilani ya mwaka 2015 mpaka sasa sijajua hatua ya Serikali katika kutekeleza ahadi hiyo imefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema kwenye majibu mengine barabara aliyoitaja iko kwenye Ilani na imeahidiwa na viongozi wa Kitaifa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kiruswa kwamba ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami utategemea na upatikanaji wa fedha na kadri Serikali tunavyoendelea kupata fedha nataka kukuhakikishia kwamba ni azma ya Serikali kuijenga hiyo barabara ikiwa ni pamoja na kutimizia ahadi za viongozi kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, tuvute tu subira, cha msingi tuendelee kufanya makusanyo ya fedha. Basi tutakapopata, hizo barabara zitajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa, barabara hii ni muhimu sana kwa ajili ya usafirishaji wa zao la korosho na kwa kuwa bajeti ya mwaka jana zilitengwa kiasi cha fedha na mwaka huu imetengwa bilioni tatu, naomba sasa nijue Je, ni lini Serikali itatangaza barabara hii ili apatikane Mkandarasi wa kuanza kipande kilichobaki cha kilometa 110.

Pili, kwakuwa kilometa 50 ambazo zimeshajengwa kwa awamu ya kwanza bado kuna kazi chache zimebaki Serikali inatuhakikishia mpaka lini kipande hiki kitakuwa kimekamilika kwa asilimia 100? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imetengewa fedha ambayo mara tu fedha itakapoanza kutumika za bajeti ambayo imepitishwa na Bunge lako barabara hii itatangazwa ili ianze kuendelea kipande cha Mnivata Tandahimba kwenda Newala, ameuliza barabara ambayo imejengwa ya Mtwara hadi Mnivata yenye kilometa 50 ni kweli haijakamilika kabisa lakini tumetenga shilingi bilioni Tatu kwa ajili ya kukamilisha barabara hiyo. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa barabara ya Mwigumbi Maswa imejengwa chini ya kiwango na imeanza kubomoka bomoka. Je, ni lini Serikali itarudia ujenzi huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther, Mbunge kama Mheshimiwa Naibu Spika, ni kawaida barabara zikishajengwa baada ya muda hasa muda wake unapokuwa umekwisha zinachakaa na hivyo kufanyiwa mategenezo kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo itaingizwa kwenye mpango wa ujenzi mara tu fedha itakapopatikana hasa katika awamu tunazoziendea, kwa sababu ni taratibu kwamba tunafanya tathmini kuangalia gharama halafu barabara hiyo itafanyiwa rehabilitation kubwa. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ya Tandahimba ni barabara ya muda mrefu sana imeahidiwa kwa muda mrefu sana tangu wakati wa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Serikali itakuwa imeamua lini kufanya kwa vitendo kutimiza ahadi zake kwa sababu barabara hii ni ya muda mrefu sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Mchungahela Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii imeahidiwa muda mrefu lakini Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara hii tayari Serikali imeshaanza kutekeleza kwa vitendo ambapo kilometa 50 zimeshajengwa na katika bajeti tunayoenda, bado tunaendelea tumetenga Billioni tatu kwa ajili ya kuanza barabara hii ya Mnivata kwenda Tandahimba. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mara bajeti itakapoanza kutekelezwa barabara hii itatangazwa na itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya kujenga barabara katika Mji Mdogo wa Karatu kwa kiwango cha lami toka Serikali ya Awamu ya Nne na Awamu ya Tano.

Je, ni lini sasa ahadi hiyo itatekelezwa kujenga kilometa 10 za lami katika mji dogo wa Karatu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara za Mjini Karatu zitajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha kadri Serikali itakavyopata fedha. Kwa hiyo, nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara yangu ya Ujenzi na Uchukuzi ikisaidiana na Wizara ya TAMISEMI tutahakikisha kwamba barabara hizi ambazo ni ahadi za viongozi na zipo kwenye Ilani zinajengwa kwa kiwango cha lami kama zilivyoahidiwa. Ahsante.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa niulize swali moja la nyongeza.

Barabara ya kutoka Katumba - Suma – Mwakareli - Luwanga - Mbambo mpaka Tukuyu yenye urefu wa Kilometa 82, imeanza kujengwa kipande cha kutoka Luhangwa – Mbambo – Tukuyu.

Je, ni lini kipande cha kutoka Luhangwa - Mwakareli - Suma - Katumba kitajengwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakibete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni mwendelezo wa ujenzi ambao unaendelea, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti hii kuna fedha ambayo imetengwa ambapo barabara hii ya Katumba hadi Luhangwa itaendelea kujengwa, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Busokelo pamoja na wananchi wa Busokelo kwamba barabara hii itaendelea kujengwa kadri fedha itakapokuwa inapatikana na tayari imeshaanza kwa hiyo Serikali itaendelea kuijenga barabara hii. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Barabara ya Bugene, Karagwe kupitia pori la Kimisi hadi Ngara Mheshimiwa Hayati Magufuli akiwa Karagwe mwaka huu mwezi wa Januari alitangaza ianzwe kuwekwa lami naomba kujua utekelezaji wake umefikia wapi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo ni kweli barabara hii iliahidiwa na ilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli barabara hii imetengewa fedha katika bajeti iliyopitishwa kwa hiyo itakuwa ni kati ya barabara ambazo zitaanza kutekelezwa kujengwa kwa kiwango cha lami mara bajeti itakavyoanza kutumika ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri majibu ambayo yana matumaini. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nje ya shughuli za kiuchumi na kibiashara ambazo wananchi wa Jimbo la Rorya watafaidika kutokana na urekebishwaji wa bandari hii, lakini pia ni pamoja na shughuli za kiusalama, hasa ukizingatia bandari hii iko mpakani kati ya nchi mbili.

Nilitaka nijue tu, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ni lini sasa bandari hii itaweza kutengewa fedha ili ianze kurekebishwa kama vile ambavyo swali la msingi limekuwa hasa ukizingatia bado hatujafanya hata ule upembuzi yakinifu kujua gharama za ujenzi wa bandari hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jafari Chege Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jibu langu la msingi nilisema kuwa Bandari ya Sota ni kati ya bandari ambazo bado hazijawa rasmi lakini zimetambuliwa na Serikali ili ziweze kurasimishwa. Kwa hiyo isingekuwa rahisi kutenga fedha kupeleka kwenye bandari ambayo bado haijarasimishwa; na ndiyo maana tumesema kwaajili urasimishaji tathmini inafanyika ili hadi mwezi Agosti mwaka huu bandari hizo baada ya kuainishwa na kuona zina sifa zitarasimishwa na baada ya hapo fedha itatengwa kwa ajili ya kuzijenga ili ziweze kuwa rasmi ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

La kwanza, kwa kuwa Serikali imesema upembuzi yakinifu wa barabara ya Katesh – Hydom unakamilika Juni, yaani mwezi huu; na kwasababu mfumo wa sasa ni wa kusanifu na kujenga. Je, baada ya mwezi wa sita ambapo upembuzi utakamilika Serikali iko tayari kuanza ujenzi mara moja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye barabara hiyo kuna maeneo mawili korofi moja ni daraja ambalo lipo Njia Panda ya Dawar kwenye hiyo barabara ya kwenda Hydom, lakini lingine ni ule Mlima Chavda ambao unakwaza usafiri na usafirishaji kwa kata za Bassodesh, Garawja, Hirbadaw, Getanuwas, Bassotu, Murbadau, Dawar yenyewe na Mogitu na mara nyingi wananchi wamekuwa wakipoteza maisha yao na kupoteza mali.

Je, Serikali itakuwa iko tayari sasa kuweka lami wakati tukitarajia ujenzi uanze kwenye eneo la Mlima Chavda na kujenga daraja imara pale kwenye ule mto uliopo kwenye njia panda ya Dawar?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Samwel Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna aina mbili, ya usanifu na kujenga ama kusanifu halafu baadaye kujenga. Kwa kuwa tayari tunafanya upembuzi yakinifu, itategemea na upatikanaji wa fedha kama utaruhusu tufanye utaratibu wa kusanifu na kujenga. Lakini kama fedha itakuwa haipo, kwa maana ya bajeti ya mwaka tunaoanza kutekeleza baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu tutafanya usanifu wa kina ili barabara hiyo sasa iwe tayari kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi wa kiwango cha lami kwa hela hiyo ya mfadhili kutoka benki ya Ujerumani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu daraja na maeneo korofi tayari tulishatoa taarifa kwa mameneja wote barabara zote ambazo zina maeneo korofi waweze kuyaainisha ili tuweze kuyafanyia mkakati wa kuyatengeneza si tu kwa barabara hii ya Hydom – Katesh bali ni pamoja na barabara zote ili tuweze kuyatengeneza, hata ikiwezekana kuweka lami nyepesi ili yaweze kupitika kwa kiwango chote. Kuhusu madaraja wataalamu wako barabarani wakiwa wanaangalia uharibifu wa madaraja hayo yote na kuweza kuyatengeneza ili baada ya kipindi hiki cha mvua kukatika basi barabara zote ziweze kupitika bila kuleta bugudha. Ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Dareda, Bashnet na Dongobesh, kwa kuwa barabara hii inaunganisha wilaya mbili wilaya ya Mbulu na Babati lakini vile vile itaunganisha halmashauri mbili ambazo zinahamia makao mapya halmashauri ya wilaya ya Mbulu inayohamia Dongobesh na halmashauri ya wilaya ya Babati ambayo sasa inahamia Dareda? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yustina Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo. Barabara ya Dongobesh Dareda ni barabara muhimu ambayo tayari Serikali imeshakamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na hivyo Serikali kwa sasa inatafuta fedha ili barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mara fedha itakapopatikana kama ambavyo imeainishwa basi katika mpango huu wa miaka mitano ni kati ya barabara ambazo ziko kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwenye Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wakazi wa Mtwara, Lindi pamoja na Ruvuma tunalazimika kufika Dar es Salaam kabla ya kuja Dodoma ambako ndiko Makao Makuu ya nchi. Lakini kimsingi kuna barabara inayoanzia Songea barabara nyingine inaanzia Masasi, Nachingwea, Liwale, Lupilo inakuja kutokea Morogoro, Ifakara, Malinyi ili kuweza kufika Dodoma kirahisi badala ya kutulazimisha tufike kwanza Dar es Salaam ndipo tuje Dodoma.

Sasa swali langu kwa Serikali kutokana na umuhimu wa barabara hii kwa watu wa mikoa ya Mtwara, Lindi na Ruvuma ili tuweze kufika kirahisi Makao Makuu ya nchi ambako ni Dodoma, ni lini itatengenezwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara anayoitaja ni barabara kuu; siyo barabara ya mkoa, ni barabara kuu, ambayo kama nimemuelewa ni hii barabara ambayo inaoanzia Lumecha, Londo, Kilosa kwa Mpepo, Malinyi, Ifakara hadi Mikumi ambayo nadhani inaunganisha mikoa ya Mtwara, Lindi na Songea kuja Makao Makuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii iko kwenye mpango, na kama ameangalia bajeti tayari, na baadhi ya maeneo kuanzia tumejenga Daraja lile la Magufuli pale Mto Kilombero lakini pia kuna kipande cha lami ambacho kinajengwa kati ya Kidatu kuja Ifakara, na sasa ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuendelea na barabara kuanzia Lupilo kwenda huku Kilosa kwa Mpepo hadi kuunganisha huku Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachotakiwa tu ni fedha kupatikana halafu tukamilishe hiyo barabara kuu ambayo kwa kweli imekuwa ni hitaji kubwa sana kwa wananchi na Wabunge wa mikoa ya kusini ambayo ni ya Ruvuma, Mtwara, Lindi na Morogoro yenyewe. Ahsante.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni barabara muhimu sana kwa ulinzi wa nchi yetu hasa kwa upande wa Tanzania na Malawi, pamoja na hayo kuna barabara muhimu sana ambayo kwa uchumi wa Kyela inafaa ijengwe mara moja.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri ni lini barabara ya Ibanda – Itungi – Poti itaanza kujengwa rasmi?

Swali la pili, wakati wa ujenzi wa barabara ya Kikusya – Matema kuna madaraja ya chuma yaliyokuwepo kwenye Mto Lufilyo Nambaka yalitolewa. Je, Mheshimiwa Waziri, kwa sababu ya uhaba wa madaraja na watu wanaotembea kilometa nyingi kufuata daraja lilipo, Serikali haioni kwamba ni muhimu sasa madaraja yale yarudishwe Kyela ili yapelekwe sehemu zenye uhitaji za Ilondo, Ipande na sehemu za pale Ngorwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Anyigulile Mlaghila, Mbunge wa Kyela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Ibanda – Itungi – Poti imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami na naamimi tayari maandalizi yako ili iweze kutangazwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Kyela waiamini Serikali na hata akienda kwenye vitabu vyetu vya bajeti tumeonesha fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili haya madaraja ambayo anayasema. Madaraja haya ya chuma ni madaraja ambayo yanatumika kwa ajili ya kutumika pale panapotokea dharura. Kwa hiyo, madaraja anayoyasema ni kweli yalikuwepo lakini yalishapelekwa Katavi kwa ajili ya koa changamoto ambayo ilitokea. Kwa hiyo, kupitia Bunge lako Tukufu nimuagize Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mbeya aende akafanye tathmini halafu tuone kama tutapata madaraja sehemu nyingine tuweze kurejesha mawasiliano ili kuwapunguzia adha wananchi ambao wanakwenda mbali kwa ajili ya kupata huduma ya usafiri. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na tofauti kubwa kati ya miradi ya upembuzi yakinifu wa barabara zetu ukilinganisha na ujenzi, kwa sababu zipo barabara ambazo zimefanyiwa upembuzi yakinifu tangu mwaka 2012 na bado hazijajengwa.

Je, Serikali haioni kwamba ipunguze miradi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili barabara ambazo zimeshafanyiwa upembuzi yakinifu kwanza zijengwe, kwa sababu haiwezekani mwaka 2012 ifanyiwe upembuzi halafu uje kuijenga 2025 useme kwamba utaijengwa kwa data zile zile, ni lazima itabidi ujenge kwa data zingine.

Je, huoni kama Serikali inapoteza fedha nyingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana nae kwamba tukifanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa muda inakuwa ni gharama kwa sababu itabidi tuje turudie, lakini azma ya Serikali wakati tunafanya upembuzi na usanifu wa kina inakuwa ni kuijenga barabara kwa kipindi hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tunavyosema kinachosumbua wakati mwingine ni upatikanaji wa fedha kwa kipindi hicho lakini ni muhimu tukafanya usanifu ili mara tunapopata fedha basi barabara hizo ziendelee kujengwa. Kwa hiyo, tutaendelea kufanya usanifu na kutafuta fedha. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Kwa kuwa tatizo lililopo Kyela ni sawasawa na tatizo lililopo katika Wilaya ya Halmashauri ya Msalala. Je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara inayotoka Busisi – Ngoma, Ngoma – Nyang’hwale, Nyang’hwale – Chela, Chela – Busangi – Kahama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara anayoisema ya kutoka Busisi – Nyang’hwale na kupita kwenye Jimbo lake ni barabara ambayo tayari imeshafanyiwa usanifu na kinachosubiri ni upatikanaji wa fedha ili barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi kwa kipindi cha miaka mitano nina uhakika zitajengwa kwa kiwango cha lami kadri fedha itakavyoendelea kupatikana. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyogeza. Kwanza kabisa nipende kuipongeza na kuishukuru Serikali kwa kutujengea hilo daraja liligharimu zaidi ya karibu bilioni 17. Tunashukuru sana. lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; Serikali sasa ina mpango gani wa kutujengea hata basi kuitengeneza hiyo barabara hata kwa kiwango cha changarawe ili wananchi waweze kupita katika barabara hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili ninaomba sasa commitment ya Serikali, kwa sababu barabara hiyo ni muhimu sana kwa uchumi wa Mikoa ya Rukwa, Katavi na Songwe. Ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum wa Mkoa wa Rukwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni kweli kwa mwaka jana na mwaka huu ilikuwa imeharibika sana. Nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, hivi ninavyoongea madaraja yote yameshajengwa, bado madaraja mawili ambayo mkandarasi anakamilisha. Kwa sasa barabara hii inapitika vizuri kwa kiwango cha changarawe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, kwamba ni lini tutaanza ujenzi; kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi. Barabara hii tunatambua umuhimu wake ndiyo maana tayari tumeshakamilisha usanifu wa kina kwenye kilomita zote, na bado kilomita 27 ambazo wako tayari wanafanyia usanifu ili barabara yote ikamilike kwa usanifu na baada ya hapo ndipo ujenzi kwa kiwango cha lami utaanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa niaba ya Wizara nimshukuru kwamba ameipongeza Serikali kwa kujenga Daraja la Mto Momba ambalo lilikuwa ni kikwazo kikubwa. Hiyo ndiyo adhma ya Serikali; na sasa mizigo yote kutoka Rukwa inapita daraja la Momba kwenye Mlowo. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa
Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya mchepuo ya Morogoro Manispaa ambayo Mheshimiwa Naibu Spika unaifahamu na unaitumia kila mara unapokwenda Dar es Salaam ili kupunguza msongamano wa magari pale Msamvu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ishengoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayosema ambayo itakuwa barabara ya by-pass ni barabara ambayo muhimu, binafsi nimepita na Mheshimiwa Ishengoma tumeongea naye. Ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu na tutaingiza kwenye mpango ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kupunguza msongamano wa kupita magari yote katikati ya Mji wa Morogoro. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Ishengoma kwamba mpango huo upo na katika siku zinazokuja kadri ya fedha zitakapopatikana barabara hii itajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kuna barabara ambayo inatoka Lumecha – Kitanda, Londo inakwenda mpaka Malinyi kutokea Lupilo, Ifakara na ipo katika Ilani ya Uchaguzi na barabara ile ya Serikali Kuu.

Je, Serikali inaweza ika-concentrate kuanza kuifungua ile barabara kutokea Kitanda – Londo mpaka Kilosa kwa Mpepo mpaka Malinyi ili ianze kupitika wakati utaratibu wa kuijenga kwa lami unaendelea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoisema ya Lumecha – Londo Kilosa kwa Mpepo – Malinyi hadi Ifakara na Mikumi ni barabara kuu kama alivyoisema. Tunafikiria kuifungua barabara hii ili iweze kutumia, na hasa kuanza na kipande ambacho kina miinuko mikali kati ya Londo na Kilosa kwa Mpepo. Ikishafunguka nadhani itapitika kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge avute subira Serikali itafute fedha ili hapo paweze kukamilika na kupatengeneza vizuri, kwa sababu ndiyo changamoto kubwa ya hiyo barabara kushindwa kupitika muda wote wa mwaka. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Iko nia ya Serikali ya kujenga barabara ya kutoka Mkiwa kwenda Noranga kilometa 56.9 ambayo ilikuwa imetangazwa mwaka 2017, na sasa hivi katika bajeti iliyopita alisema kwamba wataitangaza. Je, ni lini sasa barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Massare kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara iliyotajwa ni barabara ambayo imepata kibali na taratibu zote zimekamilika; muda wowote itatangazwa kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Mheshimiwa Mbunge tumeongea naye mara kadhaa, pamoja na Mbunge wa Chunya Mheshimiwa Kassaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii inatarajiwa kutangazwa muda wowote kwa sababu imeshapata kila kitu na imekamilika, kwa maana ya kutangazwa. Ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali langu ni kwamba, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba Daraja la Mto Luhuhu linalounganisha Wilaya ya Nyasa na Ludewa linakamilika? Kwa sababu kwa sasa hata ile Pantoni iliyokuwa inatumika nayo imeharibika.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mhandisi Stella Manyanya Mbunge wa Nyasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, daraja analolisema linaunganisha Wilaya ya Nyasa na Wilaya ya Ludewa. Katika bajeti yetu ni kati ya madaraja ambayo yamepangiwa fedha kwa ajili ya kujengwa katika bajeti inayokuja. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mara bajeti itakapoanza kutekelezwa daraja hili litaendelezwa kujengwa ili liweze kukamilika. Ahsante.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii imekuwa ikiahidiwa na Marais watatu waliopita. Je, Serikali haioni kwamba kutotekelezwa kwa ahadi za Marais wetu watatu ni kipindi kirefu sana? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tunaishukuru Serikali kwamba kwa kipindi hiki sasa imetenga bilioni moja kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu. Je, Serikali inatuhakikishia kwamba kazi hii itaenda kufanyika na kukamilika kwa kiasi hiki cha fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara hii imeahidiwa na Marais watatu kama alivyosema na ni kweli ni muda mrefu, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Mkinga na wananchi wa Mkinga kwamba wawe na imani na Serikali na ndiyo maana hata fedha tumeonesha kiasi ambacho tumekitenga ili kutimiza ahadi hizo za Marais na awe na imani sana na Awamu hii ya Sita inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Naomba nimhakikishie kwamba itatekelezwa kama tulivyoahidi na tulivyopanga kwenye bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; nimhakikishie kwamba bajeti iliyotengwa kwa maana ya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina itatosha kufanya kazi hii na kama ilivyopangwa kazi hii ya usanifu na upembuzi yakinifu itakamilika, ahsante. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi, viongozi wetu wa Kitaifa kwa nyakati mbalimbali wamefanya ziara ndani ya Wilaya ya Misenyi na kuahidi ujenzi wa barabara za lami. Barabara ya Mutukula kwenda Minziro lakini vilevile barabara kutoka Kadieli Kata ya Ishozi mpaka Gela njia panda. Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi za viongozi wetu wapendwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Florent Kyombo, Mbunge wa Misenyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara ya Mtukula hadi Minziro iliahidiwa na anakubaliana na mimi kwamba kuna kazi tayari imeshanza. Baada ya kukamilisha kwa kiwango cha changarawe na kuifungua basi tutafanya kazi ya pili itakuwa ni kuisanifu kwa ajili ya kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya pili ni barabara ambayo tayari ameshakuja mara kadhaa ofisini ni barabara ambayo ilikuwa inahudumiwa na Wakala wa Barabara (TARURA) na tayari tunafanya mawasiliano na wenzetu ili tuone namna ya kuipandisha hadhi lakini itategemea na wao watakavyoleta mapendekezo yao ili barabara hiyo kwa umuhimu wake iweze kuchukuliwa na TANROADS kama itakuwa imekidhi vigezo. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna ahadi ya muda mrefu ya kujenga kwa kiwango cha lami barabara inayotoka Karatu – Kilimapunda – Mbulu, ahadi hii imekuwa ni ya muda mrefu sana.

Je, ni lini sasa Serikali mtatekeleza ahadi hiyo kwa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara aliyoitaja ya kuanzia Karatu kuja Mbulu ni ahadi ya muda mrefu, lakini nataka nimhakikishie kwamba katika bajeti ijayo lakini hata mwaka huu barabara hii itatangazwa mara moja kuanzia kipande cha Mbulu kwenda Haydom ambayo ni sehemu ya barabara hiyo. Kwa hiyo, tayari Serikali imeanza kutekeleza hiyo ahadi. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hiii ndiyo ile barabara ambayo nilitaka kuruka somersault humu ndani. Kwanza niishukuru Serikali kwa kutangaza hizi kilometa 25.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kwenye bajeti ya Serikali ziko kilometa 50;

Je, ni lini unatangaza tena slot iliyobaki ya kilometa 25?

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa kuwa amesema barabara hii ina kilometa 70,

Je, kilometa 20 zinazobaki point tano atatangaza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei Grerory Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini, kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru kwanza leo hajataka kuruka sarakasi. Na kama alivyoahidi Mheshimiwa Waziri wakati wa bajeti kwamba barabara hizi zitatangazwa ni kweli zimetangazwa, na hizo kilomita 25 zinaanza kujengwa kwa bajeti ya mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti ya mwaka tutakayoanza Julai pia kuna fedha imetengwa. Kwa hiyo tutaendelea na ujenzi kadri fedha itakapopatikana, lakini kwenye bajeti pia tumetenga. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri fedha itakapopatikana kilomita zote na barabara yote hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante sana.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Sibiti hadi Hydom kwa kiwango cha lami kwa sababu tayari ipo kwenye bajeti? Ahsante (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyouliza Mheshimiwa Flatei ndio mwendelezo wa barabara kutoka Hydom kwenda Daraja la Sibiti. Ni barabara ambayo inafanya kama kilomita 300 na kitu ambayo inaanzia Kolandoto, Lalago, Sibiti, Hydom, Mbulu hadi Karatu. Tayari tumeshaanza ujenzi, kwa maana ya daraja na kilomita zake takriban 25; na kwa hiyo kadri tutakavyoendelea kupata hela barabara hii tutaiunganisha yote kuwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, kwa kuwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishafanyika wa daraja la Sanza.

Je, nini commitment ya Serikali kuhakikisha kwamba inaanza kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa kipande cha barabara ambacho kitaunganisha daraja hilo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, ni lini Serikali itawamalizia kuwalipa fidia wananchi wa vijiji vya Sanza Chicheho na Ikasi ili ujenzi wa daraja uweze kuanza? Ahsante sana (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu langu la msingi, ni kwamba tayari tumeshakamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa daraja na ujenzi huo utaanza mara moja, ikiwa ni pamoja na approach roads zenye urefu wa kilometa tisa upande wa Singida na kilometa tano nukta kadhaa upande wa Dodoma kwa ajili ya kuondoa changamoto iliyokuwepo kwa sababu hilo daraja liko chini. Kwa hiyo ujenzi utaanza mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la fidia; daraja hili limehamishwa mahali lilipokuwa na barabara inajengwa upya sehemu ya hilo daraja. Tayari fidia, atakubaliana nami Mheshimiwa Mbunge, Wizara na Serikali tumeshalipa zaidi ya milioni 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya wananchi kulalamika tumefanya tathmini upya na kuona kwamba zinahitajika si zaidi ya milioni 65. Tayari mchakato wa kupata hizo fedha unaendelea ili kabla ya kuanza ujenzi tumalize kwanza kuwalipa wananchi fidia halafu tutaanza ujenzi wa daraja hilo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Manyoni kwamba fidia tayari tumeshafanya tathmini upya, tutawalipa, halafu tutaanza ujenzi wa hilo daraja na hizo barabara zake. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwanza, naomba niipongeze Serikali kwa kutangaza barabara ambayo nilikuwa naipigania hapa Bungeni kwa muda mrefu ya kipande cha kilometa 25 kutoka Itigi kuelekea Noranga. Sasa, je, Serikali iko tayari kuongeza kipande kingine katika bajeti ijayo ya 2021/2022 angalau kufanya urefu uwe wa kutoshatosha? Barabara hii ni ndefu, ina kilometa 219.

NAIBU SPIKA: Unamaanisha bajeti ya 2022/2023 au? Kwa sababu hii si ndiyo tumetoka kuijadili sasa hivi?

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, hapana, namaanisha bajeti iliyotangazwa ni hii ambayo inaishia Juni. Je, kuanzia Julai 2021/2022, Serikali iko tayari kuongeza kipande kingine ili barabara hii iweze kufanya vizuri zaidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahaya Massare kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara zilizotangazwa zimetangazwa kwa bajeti ambayo tunaendelea kuitekeleza kabla ya tarehe 30 Juni na barabara anayoisema pia tumeitengea fedha kwa bajeti tutakayoanza kutekeleza Julai. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea na ujenzi kwa kipande kinachoendelea mpaka barabara itakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo bajeti tuliyotangaza ni kwa mwaka huu tunaoendelea nao kabla ya Juni, 30, lakini tumetenga pia fedha kwa ajili ya bajeti tunayoanza 2021/2022. Ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nina maswali mawili tu ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Kibena Stop Lupembe kutokea Madeke ambayo inaunganisha Mkoa wa Njombe na Morogoro? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; ni lini Serikali itajenga kwa haraka barabara ya Makete ambayo inapita Hifadhi ya Kituro kutokea Mbeya. Sababu barabara zote hizi zina umuhimu kwa Mkoa wetu wa Njombe na zitaongeza uchumi wa Mkoa wa Njombe kwenye masuala ya utalii, lakini vilevile kwenye masuala ya biashara, naomba nipate majibu ya maswali haya. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kibena - Kona kwenda Madeke ambayo inakuja kutokezea Mlimba, Ifakara ni barabara ambayo kwenye bajeti hii imetengewa fedha na itaanza kujengwa katika bajeti tunayoanza. Hali kadhalika, barabara aliyoitaja ya Makete - Isyonje kwenda Mbeya pia imepangiwa bajeti na itatangazwa katika mwaka wa fedha ujao. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge barabara zote barabara zote mbili alizozitaja zipo na zimepangiwa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa mwaka ujao wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Ni lini Serikali itakamilisha barabara ya Iringa bypass kwa kilometa 6.8 zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara uliyoitaja ya kilometa
6.9 ni barabara muhimu ambayo itatuondolea adha pale ambapo changamoto ikitokea kati ya Ruaha na Mjini pakikwama basi mji unakuwa umefunga. Na Mheshimiwa Mbunge anajua kwamba tayari tumeshaanza na katika bajeti tunayoanza, barabara hii utaendelea; lengo ikiwa ni kukamilisha hizo kilometa zilizobaki kwa ajili ya kuondoa hizo changamoto, ahsante.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali moja la nyongeza.

Umuhimu wa barabara hii umeongezeka baada ya ule mradi mkubwa wa bomba la mafuta kutoka Uganda mpaka Tanga, umeamua kujenga ile kambi kubwa itakayoandaa mabomba yote yatakayofukiwa njia nzima pembeni ya barabara hii na kwa kuwa wasimamizi wa mradi huu wale ECOP wana package ya miundombinu ya kuboresha barabara; na kwa kuwa kuna kakipande kama kilometa 50 mpaka 60 kutoka Nzega - Itobo mpaka kwenye ile kambi ambako mabomba yatapita.

Je, Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi haioni umuhimu wa kukaa na hawa wasimamizi wa mradi huu wa ECOP kwa sababu na wenyewe wana package ya miundombinu wakashirikiana ili kipande hiki cha kilometa 50 mpaka 60 cha Nzega - Itobo mpaka Sojo ambako ni kipande katika barabara hii hii, wakashirikiana na wakapunguza gharama upande wa Serikali na huu mradi ukatoa fedha zake ili kukamilisha barabara hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Zedi, Mbunge wa Bukene kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Zedi kwa mchango huo na mimi nimhakikishie Wizara pamoja na hawa watu wa ECOP tutakaa nao kuona uwezekano wa kujenga hiki kipande cha kilometa 50 hadi 60 kutoka Itobo hadi Nzega ili kuweza kurahisisha utengenezaji wa hili bomba, kwa hiyo mimi binafsi nimhakikishie Mheshimiwa nitafika Jimboni kwake na tuweze kuangalia uwezekano huo, ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; kwa kuwa viongozi wa Kitaifa waliahidi pale Makambako kutengeneza barabara kilometa mbili za lami pale mjini. Ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ya viongozi wa Kitaifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema sisi kama Wizara na Serikali kazi yetu kwakweli ni kuhakikisha kwamba zile ahadi zote zilizoahidiwa na viongozi wa chama na hasa ngazi ya kitaifa zinatekelezwa, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako ahadi hizo zitatekelezwa kulingana na fedha zitakapoendelea kupatikana na hasa katika kipindi hiki cha miaka mitano ambacho ndicho tumekianza, ahsante. (Makofi)
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona nilitaka kuulizwa swali la nyongeza kwamba viporo vya barabara zinazounganisha mikoa ni pamoja na viporo vya barabara ya eneo la Malagalasi - Uvinza kilometa 51 na kiporo cha barabara inayotoka Tabora kuja Nguruka kilometa 40; nataka nijue Serikali ni lini ujenzi wa viporo hivi kukamilisha barabara inayounganisha Mkoa wa Kigoma na Tabora vitakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara alizozitaja za Kaliua mpaka Chagu yenye kilometa kama 36 tayari mkandarasi yupo site na amepiga kambi Kijiji cha Usinge, kwa hiyo ujenzi unaanza, lakini katika barabara ambazo zimetangazwa mwezi huu ambazo zinafadhiliwa na Mfuko wa OPEC kutoka Malagalasi hadi Uvinza yenye kilometa 51.3 tayari barabara hii imeshatangazwa kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi kwa kiwango la lami na hivyo Mheshimiwa Kilumbe na wananchi wa Kigoma baada ya muda si mrefu kuanzia Dodoma mpaka Kigoma itakuwa ni kwa lami tu bila kugusana na vumbi, ahsante. (Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante barabara ya kutoka Amkeni – Kitangali hadi Mtama yenye kilomita 74 ndiyo barabara pekee inayofungua mji wa Newala na maeneo mengine kuelekea Dar es Salaam hadi kuja huku Dodoma. Nakubaliana na Mheshimiwa Waziri kwamba fedha zitatengwa kwa awamu lakini ikumbukwe kwamba wilaya hii ni ya muda mrefu tangu 1952 hadi leo haina barabara ya uhakika. Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kutosha ili barabara hii iweze kukamilika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kutokana na changamoto za ubovu wa hii barabara wafanyabiashara wengi wa usafirishaji wanakwama kupeleka vyombo vyao vya usafiri kwa hofu ya uharibifu wa vyombo vyao na wananchi wanateseka na usafiri kwa sababu ya ubovu wa barabara. Je, Serikali haioni kwamba inarudisha nyuma jitihada zake za ajira kupitia sekta zisizo rasmi hasa usafirishaji? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi barabara hii ni kweli ni ya muhimu sana kwa mkoa wa Mtwara ambayo inaunganisha mkoa wa Lindi. Lakini kwa kulitambua hilo Wizara ya Ujenzi kupitia TANROAD inajenga maeneo korofi yote kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba maeneo mengi korofi yamejengwa kwa kiwango cha lami na hata katika mwaka huu wa fedha tunaoendea kuna fedha imetengwa kwa ajili ya kujenga kwa kiwango cha lami yale maeneo yote korofi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, ambalo linafanana hili jibu la kwanza kwa sababu ya kutambua ule ubovu kwenye hii barabara ndiyo maana sasa TANROADS Mkoa wa Mtwara unafanya kila jitihada kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika muda wote na kuhakikisha kwamba maeneo korofi yote yanawekewa lami ili barabara hii iweze kupitika muda wote wa mwaka ahsante.
MHE. NAGHENJWA L KABOYOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa katika mwaka wa fedha huu 2021 Serikali ilisema imetenga bilioni 5 kwa ajili ya kujenga barabara ya kutoka Same Kisiwani mpaka Mkomazi kwa kiwango cha lami. Je, fedha hiyo itatolewa lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kaboyoka Viti Maalum kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema fedha hii kwa kujenga kwa kuanza kwa kiwango cha lami Same hadi Mkomazi ambapo tumetenga bilioni 5 fedha itaanza kutoka mara bajeti itakapoanza kutumika ya mwaka 2021/2022, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa kuwa barabara hii ya Mkwiti – Amkeni inayounganisha mkoa wa Lindi na Mtwara tatizo lake linafanana kabisa na barabara ya Singida Simiyu inayoanzia Iguguno na kwa kuwa Serikali imevunja nyumba za wananchi wa Iguguno hivi karibuni.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi barabara hii hasa kuanzia Iguguno mpaka Nduguti?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ni barabara ambazo zitajengwa katika kipindi hiki cha miaka mitano na itategemea na upatikanaji wa fedha hatuwezi leo tukaahidi kwamba itaanza mwaka ujao kwa sababu haijaingia kwenye mpango. Lakini nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika miaka inayokuja ya bajeti itaingizwa kwenye mpango ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa ni kuanzia na upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na hatimaye kujenga kwa kiwango cha lami ahsante.
MHE. CHRISTOPHER O. OLE-SENDEKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa kuwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara inayotoka Arusha, Simanjiro, Kiteto, Kongwa umekamilika na ni ahadi ya muda mrefu ya ilani za uchaguzi kadhaa. Je, ni lini Serikali Sikivu ya CCM itaanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sendeka Mbunge wa Simanjiro kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii aliyoitaja ni barabara muhimu sana hasa kwa mikoa ya Arusha Manyara na Dodoma na nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni kati ya barabara ambazo ziko kwenye mpango na kwa kuwa usanifu umeshakamilika Serikali inatafuta fedha ili barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami katika awamu ambayo ime...

MWENYEKITI: Ahsante ameshakuelewa barabara inajengwa Mheshimiwa Naibu Waziri.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuwa barabara ya kutoka Busisi Nyang’wale kwenda Kahama imeahidiwa na viongozi wakuu wa nchi kujengwa kwa kiwango cha lami. Ni lini Serikali itaanza upembuzi yakinifu na ujenzi wa barabara hiyo kuanza mara moja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amar Mbunge wa Nyang’wale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni barabara ambayo katika ilani ya chama itafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika kipindi hiki. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute Subira fedha ikipatikana ya Serikali tutafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kama fedha itaruhusu basi tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami ahsante.
MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, swali langu la nyongeza, barabara ya kutoka Mbalizi mpaka Mkwajuni sasa ni miaka 15 imekuwa ikiahidiwa na Waheshimiwa Marais wanaokuja kupiga kampeni kule Mheshimiwa Dkt. Kikwete alituahidi miaka 10 ikapita bila kujenga, Mheshimiwa Rais marehemu Mungu amlaze mahali pema peponi Mheshimiwa JPM naye aliahidi…

MWENYEKITI: Usilete ufundi kwenye swali uliza swali moja kwa moja. (Kicheko)

MHE. PHILIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Waziri ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kutoka Mbalizi mpaka Mkwajuni kwa sababu nimekuwa nikiahidiwa miaka mingi? Na upembuzi yakinifu tayari umeshaisha kabisa naomba majibu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Phillipo Mulugo Mbunge wa Songwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikubaliane kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa Mkoa wa Songwe lakini pia kwa wilaya ya Chunya na wilaya ya Songwe. Barabara hii imeahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami lakini bado nimpe pole sana Mheshimiwa kwa sababu katika kipindi chote hiki ilikuwa haipitiki kwa sababu ya mvua lakini TANROADS mkoa wa Songwe ilifanya jitihada kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mulugo kwamba katika kipindi hiki cha miaka mitano kama ilivyoahidiwa na tunavyotekeleza ilani za viongozi wakuu wa Serikali barabara hii nayo itafanyiwa kazi kwa maana ya kujengwa kwa kiwango cha lami kadri fedha itakavyopatikana, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi barabara ya Mafinga Mgololo ambayo ni kiungo muhimu sana cha uchumi katika uchumi wa Mufindi na Iringa imeahidiwa toka ilani ya uchaguzi 2005 ninauliza Serikali. Je, wakati jitihada za kujenga kwa kiwango cha lami zinaendelea Serikali iko tayari kushughulikia na maeneo korofi kama vile Itulavanu, Mtili na pale mlima wa Kalinga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chami Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kupitia Bunge hili nimuagize Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa aende akaangalie maeneo hayo korofi aweze kufanya tathmini ili yale maeneo korofi tuweze kutafuta fedha ili barabara hiyo iweze kutengenezwa maeneo korofi yaweze kupitika muda wote wa mwaka. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Serikali ilishapitisha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami kutoka Geita kwenda Nyang’hwale, tulikuwa tukipewa kilomita nne kila mwaka na sasa hivi tumeshajengewa zaidi ya kilomita nane; miaka miwili iliyopita hatujapewa tena hizo kilomita nne nne: -

Je, Serikali inatoa kauli gani; imeifuta hiyo barabara kwa ujenzi wa lami au la?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, alivyosema Mheshimiwa Hussein Amar Mbunge barabara ya Geita hadi Nyang’hwale ni barabara ambayo tayari imeshaanza kujengwa na Serikali haijaifuta barabara hiyo kuijenga kwa kiwango cha lami. Tumhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itaendelea kujengwa kadri fedha itakavyoendelea kupatikana. Kwa hiyo, haijaifuta na haina mpango wa kuifuta, lakini itategemea na upatikanaji wa fedha hili kuendeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa viongozi wakuu waliahidi kiwango cha kilimeta 10 katika Mji wa Karatu mwaka 2010 – 2015 na 2015 - 2020 mpaka leo hii hatuna hata kilometa moja: sasa ni lini ahadi ya viongozi wakuu itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Awack kuhusu ahadi za Viongozi wa Kitaifa ya kujenga barabara kilometa kumi katika Mji wa Babati, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kazi ya Serikali ni kujenga barabara hizo kama zilivyoahidiwa na Viongozi wa Kitaifa. Ujenzi huo kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi zitajengwa katika awamu hii ya miaka mitano. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge avute subira na kadri bajeti itakavyoruhusu, hiyo barabara ya kilomita 10 itajengwa katika Mji wa Babati. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imejiridhisha kuwa barabara ya kuanzia Dochi kupitia Ngulwi hadi Mombo ambayo ni kilometa 16 kuwa itajengwa na TANROADS: -

Je, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Shekilindi barabara ya Dochi - Mombo yenye urefu wa kilomita 16 itajengwa na TANROAD, lakini katika mpango huu kwa mwaka huu wa bajeti, barabara hii haimo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TANROADS kupitia Serikali, barabara hii katika mipango ijayo itajengwa kama ilivyoahidiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Murushaka kwenda mpaka Mrongo ni barabara ya kiuchumi kwa Mkoa wa Kagera, lakini pia ni barabara muhimu inayounganisha nchi ya Tanzania na Uganda; na kwa umuhimu wake Mheshimiwa Hayati Pombe Magufuli aliahidi ijengwe kilometa 50 za haraka. Ni lini kilometa 50 hizi zitajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara ya Mrongo yenye urefu wa kilomita 112 aliyoitaja Mheshimiwa Bilakwate ni kweli iliahidiwa na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, barabara hii imeingizwa kwenye mpango na fedha imetengwa kwa ajili ya kuanza mwaka wa fedha ujao kwa kiwango cha lami. Nadhani tumetenga kama siyo chini ya shilingi bilioni tatu kwa kuanzia. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa wa Kyerwa na wananchi wa Kyerwa, ahadi ya Mheshimiwa Rais Hayati itaanza kutelekezwa mara tutakapoanza utekelezaji wa bajeti ambayo Bunge lako imelipitisha. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimwa Spika, ahsante, kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimwa Spika, kwa kuwa fursa kama hizi mfano Ujenzi wa Mradi wa Bomba la Gesi ni fursa nzuri sana kiuchumi katika nchi na kwa kuwa Serikali imesema italipa fidia kwa ajili ya upanuzi wa uwanja huo wa Tanga, lakini je, Serikali haioni ipo haja ya dharura hata kutafuta mkopo wa dharura ili fursa hii ya ujenzi wa bomba la gesi uendane na ukarabati wa uwanja huo wa Tanga?

Mheshimwa Spika, swali la pili, kuna mchakato pia wa upanuzi wa uwanja wa Lake Manyara, Karatu ambao ni uwanja muhimu sana kwa utalii katika Kanda ya Ngorongoro – Serengeti, wananchi wale hawajalipwa fidia muda mrefu.

Je, ni lini sasa Serikali italipa fidia wananchi hawa wa Lake Manyara pale Karatu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza naamini anakusudia kusema bomba la mafuta na si bomba la gesi; kama hivyo ndivyo Serikali inatambua umuhimu wa bomba hili na ndio maana tunapoongea hivi tayari kuna watu wanafanya tathimini kwa ajili ya watu watakaopisha upanuzi wa kiwanja hiki ili uwanja huu uendane na kasi ya utekelezaji wa mradi wa bomba la mafuta la kutoka Tanga kwenda Uganda. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali inalitambua hivyo na ndio maana iko kasi kuhakikisha kwamba uwanja huu unajengwa.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kama amesikiliza kwenye jibu langu la msingi nimetaja viwanja 11 ambavyo viko katika mpango huu na katika kitabu chetu cha bajeti ambayo imepitishwa kiwanja cha Lake Manyara ni kati ya viwanja hivyo 11 ambavyo pia vinafanyika upembuzi yakinifu na usanifu wa kina unafanyika hili kuweza kuhakikisha kwamba ndege sasa zinatua uwanja huu wa Lake Manyara kwa ajili ya kuongeza shughuli za utalii eneo hili la Mkoa wa Manyara na Karatu kwa ujumla wake, ahsante.
MHE. MUSSA A. ZUNGU: Mheshimiwa Spika, mimi nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, hii barabara inayotoka Klabu ya Yanga inapita Kata ya Jangwani na Mchikichini na kuja kuunganisha kwenye barabara ya Kawawa ni barabara ambayo inachukua magari takribani 40,000 kwa siku na hali ya barabara hii ni mbaya, haipitiki, inaleta msongamano na kero kubwa sana kwa watumiaji wa barabara hii.

Je Serikali imechukuwa hatua gani kuboresha barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zungu Mbunge wa Ilala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hizi alizozitaja Mheshimiwa Zungu katika moja ya vikao alitoa kama Mwenyekiti na nimempa taarifa kwamba baada ya kulisemea hilo TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam wako site kuangalia barabara hii ili waweze kuikarabati na kuondoa mashimo yote ili changamoto ambaza zinatokea ziweze kuondolewa.

Kwa hiyo, ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuliahidi kwamba tutalifanyia kazi tumeshalifanyia kazi na TANROADS Dar es Salaam wako site kuhakikisha kwamba changamoto ambayo ipo kwenye hizi barabara inatatuliwa haraka, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba Mheshimiwa Waziri hafahamu kwamba hii ni changamoto kubwa sana kwa Jiji la Arusha na inaathiri karibuni Kata 15 Kata ya Ulolieni, Kata ya Balaha, Kata ya Sekei, Kata ya Kimandolu, Sakina, Kaloleni, Revolosi, Sombetini Osunyai, Unga Limited, Yalelai, Daraja Mbili, Mulieti, Sokonwali na Sinoni. Unaona zaidi ya nusu ya kata zote zina changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza nilikuwa naomba kufahamu ni wadau gani walioshirikishwa ikiwa Ofisi ya Mbunge haijashirikishwa, nimeongea na watu wa TARURA hawajashirikishwa, lakini na madiwani pia wa kata zinazohusika pia awajashirikishwa; kwanza ningependa kufahamu ni wadau gani ambao wameshirikishwa kwenye hii study na kwenye solution ya hili jambo?

Mheshimiwa Spika, lakini ya pili nilikuwa naomba kwa uongozi wako kwa sababu jambo hili linahusisha Wizara mbili; Wizara ya Uchukuzi pamoja na wizara ya TAMISEMI; je, Waziri haoni haja kwamba wizara hizi mbili tukafanya kikao pale Jijini Arusha, kwa kushirikisha Mkuu wa Mkoa pamoja na Mkuu wa Wilaya ili mwisho wa siku tutafute solution ya kudumu kwa wananchi wetu wa Jimbo la Arusha Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi ni kwamba baada ya kupata hii changamoto ambayo mafuriko yanasababishwa na maji kutoka mlimani na Mheshimiwa Mbunge amekuwa analifuatilia sana, Serikali imeamua kufanya study kuona namna ya kuondosha hili tatizo.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye study hii baada ya kukamilika, itakapokuwa taarifa imepatikana hatutaanza kutekeleza mradi hapo ndipo tutakaposhirikisha wadau kulingana na taarifa za study zitakavyokuwa zimeonyesha kwamba sasa tunategemea kufanya hiki na hiki.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya tafiti hiyo kukamilika wadau hawa watashirikishwa kabla ya kuanza kutekeleza huo mpango ambao utakuwa sasa umebainika kutokana na study hiyo, lakini nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi tulipojenga barabara hii ya TANROADS barabara nyingi zinazoathirika na wananchi wanaoathirika ni wa Wizara sana wanaoshughulikiwa na TARURA na TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Serikali tunafanya kazi kama timu tutaongea na TAMISEMI na si TAMISEMI tu tu pengine hata ofisi za mazingira na hata watu wa kilimo ambao pengine huko wanasababisha miundombinu yetu kuharibika. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mbunge kwamba kama Serikali tunafanya pamoja kuhakikisha changamoto hii tunaiondoa, ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi.

Mheshimiwa Spika, msongamano huu wa magari katika Mji wa Tuduma haujaathiri tu magari yanayopita mpakani, lakini umeathiri wananchi na usafiri wa daladala, na wananchi wote hata wanaokwenda mikoa ya jirani. Lakini Mheshimiwa Rais, Marehemu Dkt. Magufuli, alipofika wakati wa kampeni aliahidi kilometa 10 za lami kwa ajili ya kupunguza huu msongamano kwa ajili ya kujenga njia za pembezoni na za mchepuko. Sasa nini kauli ya Serikali kuhusu ahadi hii ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa ya kilometa kumi za lami ili kupunguza msongamano katika Mji wa Tunduma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tunakubali kwamba ahadi hiyo ilitolewa na Mheshimiwa Rais. Lakini kwa kutambua changamoto ya msongamano ambayo ipo pale Tunduma, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi ina mambo yafuatayo ili kuondoa hizo changamoto za msongamano.

Mheshimiwa Spika, kwanza, tunategemea kubadilisha mfumo wa mizani iliyopo iwe ni weigh in motion ambayo inachukua muda mfupi sana, pale Mpemba ambayo ni jirani, kama kilometa 10 pale Tunduma, ambayo inachukua takribani dakika moja mpaka mbili gari linakuwa limeshapita. Kwa hiyo, itakuwa ni moja ya njia za kuondoa msongamano.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, nitumie Bunge hili kusema kwamba Halmashauri ya Tunduma waweze kuongeza maegesho ili magari ambayo hayaendi kwenye Kituo cha Forodha yasiwe na sababu ya kukaa barabarani. Kwa hiyo, ni fursa kwa Halmashauri ya Tunduma kuongeza maegesho.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa tatu, ile barabara sasa hivi tunaifanyia utaratibu tuweze kupanua njia ili kuwe na lane badala kuwa na lane mbili ziwe walau ziwe hata lane nne, lakini mkakati wa nne ni kutengeneza bypass ya barabara ili magari yote ambayo yanakwenda ama yanatoka yaani yanakwenda Mkoa wa Rukwa na Mkoa wa Katavi hadi Kigoma yasiwe na sababu ya kupita Tunduma, kwa hiyo yapite pembeni ili kuruhusu hii barabara sasa iwe huru na tunaamini tukifanya hivyo tutakuwa tumepunguza sana msongamano katika njia hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza kwenye suala hili la msingi lililolenga Wizara ya Fedha.

Katika mpaka wa Namanga kuna tatizo kubwa sawa la Tunduma la msongamano wa magari ambayo wakati mwingine huchukua hata zaidi ya siku tatu yakingojea kuwa cleared yaweze kuendelea na safari na adha kubwa inayotokea ni kwamba hakuna miundombinu ya vyoo, mahali pa kuoga wale wanaokaa kwenye malori na wanachafua sana mazingira.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inampango gani wa kuhakikisha kwamba wakati mipango ya kutengeneza maeneo sahihi ya kuengesha haya malori na sisi Longido tuna sehemu TANROADS wametenga zaidi ya hekari 200 na ujenzi unaendelea, wana mpango gani wa kuhakikisha kwamba wananchi wa mipakani hawapati magonjwa ya mlipuko kwa sababu ya msongamano wa magari na hakuna miundombinu ya kijamii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, Mbunge wa Longido kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la nyongeza la Mheshimiwa Mwenisongole, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa wa Jimbo la Longido kwamba Serikali inazifahamu hizo changamoto na tupo kusaidiana na wenzetu, sisi ndiyo tunaojenga vile vituo tunayatambua hayo na tutahakikisha katika mpango wa karibu tunakwenda kuondoa hizo changamoto ikiwa ni pamoja na kujenga hiyo miundombinu ya haraka ili wananchi wasiweze kupata adha ikiwa ni pamoja na kuangalia utaratibu wa kupunguza ile misongamano kwa kujenga barabara na maegesho makubwa ili magari yatakayokuwepo kwenye foleni ni yale tu ambayo yanatakiwa kwenda kwenye Vituo vya Forodha, ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika ahsante sana, kwanza nishukuru sana kwamba wakati wa kuchangia Mpango nilielezea kutokurudhishwa kuhusu mkandarasi aliyekuwa anaweka ile lami ya kilometa 10 na amebadiliswa na speed yake sasa yule anaeendelea kwa kweli ni nzuri na inaridhisha.

Sasa maswali yangu, kwa sababu ukiangalia kuna Project ya World Bank ambayo barabara hii kilometa zote 33.6 zilikuwemo na ninafahamu kwamba Waziri wa Fedha alisaini mkataba na hawa watu wa World Bank kwa ajili ya hiyo project. Je, upatikanaji wa fedha hizo utaondoa huo ujenzi wa awamu na kufanya barabara hii iweze kujengwa yote na kukamilika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Waziri atakuwa tayari kuambatana pamoja na mimi kwenda kuangalia hasa maeneo ya milimani kwa barabara hii ambayo hayapitiki ili tuweze kupata ufumbuzi na wananchi waweze kupita vizuri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru kwa kutambua jitihada za Serikali na kwamba ni sikivu, alichokiomba tumeshakitekeleza kama Wizara. Pia nimpongeze kwa kuwapigania sana watu wa Kilolo kuhusu hii barabara, sasa majibu yangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema kwamba Waziri wa Fedha amesha saini mkataba huu na labda tu nielezee kwamba mkataba huu unafadhiliwa na Benki ya Dunia ambao umechukua muda kutokana na ukweli kwamba mradi huu ulikuwa una cover mikoa michache, kwa hiyo Serikali iliona huu mradi utanuliwe, pia ulikuwa unalenga sana barabara za changarawe, kwa hiyo, Serikali ikaona hatuwezi tukachukua fedha World Bank kwa ajili ya changarawe, kwa hiyo, kukawa na majadiliano ili kuuboresha, kwanza uchukue mikoa mingi pia uwe ni kwa kiwango cha lami ambapo ni barabara za kutoka vijijini kuunganisha na barabara za mikoa na barabara kuu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo baada ya kusaini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii kilometa zote 33 zipo kwenye mpango, na zitajengwa ndio maana tunafanya design upya kuhuisha ile design iliyokuwepo ili iendani na kiwango cha sasa cha barabara.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, mimi Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie kwamba nipo tayari kuambatana naye kwa ajili ya kwenda kuangalia hizi barabara na kuhakiki jinsi ujenzi unavyoendelea, ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, na mimi kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Iko barabara ya kiuchumi barabara ya ukombozi kwa Wilaya ya Liwale, barabara ya Nangurukuru - Liwale. Barabara hii bajeti ya mwaka jana ilitengewa fedha kwa ajili ya kufanyiwa upembuzi yakini na usanifu wa kina, na mwaka huu pia imetengwa kwenye kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Wana Liwale wangetaka kusikia, ni lini barabara hii itakwisha kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, na hatimaye kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuberi Kuchauka Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti tuliyopanga, tunauhakikia tutakamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara yote, lakini pia katika maeneo yale kofofi, tumemuagazi Meneja wa TANROADS ayape kipaumbele ili kuhakikisha kwamba yanatengenezwa vizuri ili yasiathiri kupita kipindi kile cha masika, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa kuonesha nia ya kuanza kuijenga hii barabara kwa sababu ni ahadi ya muda mrefu iliyoko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipande cha kilometa 74 ipo mito minne ya Itembe, Chobe, Lyusa na Nkoma ambayo imekuwa inakwamisha kuleta tija ya daraja la Sibiti lililogharimu shilingi bilioni 34.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kutembelea kipande hicho na kuweza kuishauri Serikali kuanza kujenga madaraja kwa fedha iliyotengwa mwaka huu wa fedha unaoanza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika barabara inayoiunganisha daraja la Sibiti kilometa 25 ambayo pia imetengewa fedha iko juu ya mbuga kali sana. Kujenga barabara hii inatakiwa ianze katika kipindi cha kiangazi. Ni nini kauli ya Serikali kuhusu kuianza barabara hii kama ilivyotengewa fedha mwaka 2021/2022? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Meatu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Leah Komanya kwamba yale ambayo tumejadili sana ulivyokuja ofisini bado yanabaki kuwa hivyo hivyo na nitaendelea kuyaeleza hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Daraja la Sibiti ambalo lina barabara ya maingilio yenye urefu wa kilometa 25 nataka nimhakikishie Mheshimiwa Komanya na wananchi wa Meatu kwamba tayari mkataba umeshasainiwa na muda wowote barabara yenye urefu wa kilometa 25 unaanza kujengwa, lakini hautajengwa kwamba ni kilometa nusu Simiyu na nusu Singida bali tutajenga zaidi upande wa Singida ambako ndiko kwenye bonde kubwa kuhakikisha kwamba barabara hiyo inapitika.

Kwa hiyo, tayari muda wowote barabara itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami ambayo pia ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu madaraja aliyoyataja naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Meatu niko tayari kwenda kuyakagua kwa sababu ni barabara ambayo imeongelewa sana, lakini nimhakikishie kwamba tayari tumeshafanya design, kwa hiyo, kinachotegemewa sasa hivi ni kupata fedha ili tutakapoanza ujenzi basi tutasubiri pia na tutategemea ushauri wake pengine ikiwezekana tuanze kwanza kujenga madaraja hayo kabla ya kujenga barabara. Kwa hiyo, nitakuja kama alivyoshauri. Ahsante sana.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Swali la kwanza, napenda kumwuliza Waziri wa Ujenzi kwamba, kwa kuwa katika mwaka 2019, Serikali ilichepusha katika Kijiji cha Njinjo, barabara ya Nangurukuru – Liwale na hivyo ililazimu kulipa fidia kwa baadhi ya wananchi ambao walikuwa na mali zao katika lile eneo ambalo limechepushwa barabara; lakini kuna wananchi wawili hadi kufikia sasa hawajalipwa fidia ya mali zao; nao ni Mama Mary Mahmoud Kiroboto pamoja na Ndugu Said Salum Karanje, ambao wanadai jumla ya shilingi 13,264,180/ =. Napenda kujua: Je, Serikali ni lini itawalipa wananchi hawa wawili haki yao ya fidia kwa ajili ya kuchepusha kipande kile cha barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, napenda kumwuliza Waziri kwamba, kwa kuwa wakati wa maadhimisho ya Kumbukizi za Vita vya Majimaji ilipotimiza miaka 100 mwaka 2010, aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete wakati ule, aliwaelekeza Wakala wa Barabara Tanzania Mkoa wa Lindi…

NAIBU SPIKA: Uliza swali lako, Mheshimiwa Ndulane.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante nashukuru. Alitoa maelekezo wafungue barabara kati ya Nandete na Nyamwage: Je, mpango huu umefikia wapi wa kufungua barabara ile ya kipande cha Nyamwage kwenda Nandete? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa, Francis Ndulane Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake amesema kwamba, kulitolewa ahadi na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tatu. Napenda tu nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa hii barabara ilitakiwa ifunguliwe maana yake haipo kwenye mtandao wa barabara za TANROAD wala za TARURA. Hivyo napenda nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imelichukua na tutawasiliana na Meneja wa TANROAD Mkoa wa Lindi ili tuweze kupata taarifa sahihi na ahadi hii ili tuweze kuanza kuitekeleza ama kama ilikwama tujue ni kwa nini ilikwama wakati ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali la pili, kama ulivyotoa maelekezo, ni swali ambalo lipo very specific na kama watu hao wapo ni bora wakaandika barua rasmi kwa TANROAD Mkoa wa Lindi, wakupe copy na sisi watupe copy ili tuweze kuliangalia, kwa sababu ni suala la watu wawili, tuweze kuliangalia kama lina changamoto gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Changamoto iliyopo kwenye barabara ya Liwale -Nangurukuru inafanana kabisa na changamoto iliyopo kwenye barabara ya Mtwara Pachani, Lusewa kwenda Nalasi mpaka Tunduru Mjini. Mwaka, 2015 aliyekuwa mgombea mwenza ambaye ni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, alitoa ahadi barabara ile kutengenezwa kwa kiwango cha lami. Nashukuru Serikali imekamilisha upembuzi yakinifu mwaka jana 2020: Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mtwara - Pachani hadi Nalasi ni barabara ambayo tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa hiyo, kinachosubiriwa sasa hivi ni Serikali kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga hii barabara. Kwa hiyo, tayari taratibu zimeshaanza, tunachosubiri tu ni fedha ipatikane. Katika Awamu hii ya miaka mitano, kama fedha itapatikana, basi itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kutekeleza hiyo ahadi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Miundombinu. Barabara ya Nangurukuru - Niwale ni mwaka wa tano inatengwa fedha kwa ajili upembuzi yakinifu na usanifu wa kina…

NAIBU SPIKA: Uliza swali. Taja barabara unayotaka ijibiwe.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, Nangurukuru - Liwale, fedha hazijawahi kuletwa tangu zinatengwa miaka yote mitano.

NAIBU SPIKA: Swali lako ni nini?

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara ya Nangurukuru - Liwale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, swali la nyongeza la mheshiiwa Kuchauko ndiyo lilikuwa swali la msingi na Serikali imetenda shilingi milioni 548.603 na tumesema taratibu zote zimekamilika na muda wowote inatangazwa.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninalo swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba commitment ya Serikali, ni lini itajenga hizi kilometa 128.5 za barabara hii kupitia Pori la Kimisi hadi Benaco Ngara kwa kiwango cha lami? Kwa sababu nilishauliza mara nyingi sana ndani ya Bunge hili, najibiwa upembuzi yakinifu, upembuzi yakinifu, sasa naomba commitment ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY
K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, Kagera kwamba siyo tena tunaongelea upembuzi yakinifu ama usanifu wa kina. Naomba nimhakikishie kwamba tupo kwenye hatua za manunuzi. Mkandarasi wa barabara hii ameshapatikana na tupo kwenye majadiliano namna ya kuanza hii barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimtoe wasiwasi kwamba jinsi anavyofuatilia tutaanza na kilometa 60 kuanzia Bugene kuelekea Kasulo, yaani Benaco. Kwa hiyo, siyo tena habari ya kubabaisha, ni habari ya ukweli kwa sababu tayari tupo kwenye hatua za manunuzi. Kwa hiyo, awe na uhakika kwamba kazi anayofanya kufuatilia, sisi tunafanya na fedha hii tayari imeshatengwa kwa ajili ya kuanza ujenzi huo. Ahsante. (Makofi)
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa barabara ya Iguguno – Sibiti yenye urefu wa kilometa 102 ina ahadi ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli Rais wa Awamu ya Tano: Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami ili kuharakisha shughuli za maendeleo kwa wananchi wa Jimbo la Iramba Mashariki na Mkoa wa Simiyu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY
K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aysharose Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ni ahadi ya viongozi wetu na pia ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Singida, Simiyu, Mara na hata Manyara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ni kati ya barabara ambazo zina barabara nyingi ambapo tayari kwenye bajeti ya mwaka uliopita tumepitisha kuanza kujenga hii barabara kwa sehemu. Ili tuanze kukamilisha hii barabara na katika hili daraja la Simiti, tayari tutakamilisha ujenzi kwa kiwango cha lami kwa barabara za maingilio. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Aysharose kwamba Serikali mwaka huu wa fedha kama tulivyoahidi kwenye bajeti na pia kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tutaanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sababu upembuzi yakinifu na usanifu wa kina tayari umeshafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nami naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali kuhusiana na barabara ya kutoka Amkeni – Kitangali hadi Mtama yenye kilometa 74.23 ambayo imeshajengwa kwa lami kwa kilometa 22.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaomba commitment ya Serikali ni lini itatafuta fedha kutoka kwa wadau wengine wa maendeleo ili barabara kipande kilichobaki kiweze kukamilishwa kwa kiwango cha lami kwa sababu Serikali imekuwa ikitenga fedha kidogo, inajenga kilometa tatu tu kwa mwaka?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupata jibu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY
K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Mtanda, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hii barabara aliyoitaja ya Amkeni kwenda Kitangali, tumekuwa tukitenga fedha kidogo kwa ajili ya ujenzi, lakini yote hii ni kutokana na uwezo wa bajeti. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya fedha kwa ajili ya kujenga barabara, siyo hii tu bali ni barabara zote, kwamba kadri fedha inavyopatikana, basi Serikali itaongeza fedha. Ndiyo maana hata tukitangaza barabara pengine kilometa tatu, lakini fedha ikipatikana Serikali hatusiti kuongeza bajeti kwa ajili ya kuendeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na barabara hii, kadri fedha itakavyopatikana, Serikali itazidi kuongeza kiasi cha fedha. Ahsante.
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nilijitahidi kuwa specific kidogo; watu wa Malinyi na Namtumbo na Ruvuma yote tunahitaji kuona Mkoa wa Morogoro na Ruvuma unaunganishwa kwa maana ya kufunguliwa. Suala la lami tutavumilia kusubiria, tunajua gharama ni kubwa, kilometa ni nyingi, lakini kuunganisha tu hata kwa kiwango cha vumbi; je, Serikali iko tayari?

Mheshimiwa Naibu Spika, kama inaridhia, iko tayari kuweka fedha kidogo kwa ajili ya barabara hiyo katika bajeti inayofuata? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Antipas Mgungusi Mbunge wa Malinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema, eneo analoliongelea lina milima mingi na linapita kwenye safu ya Mbuga ya Selous, ina urefu wa takribani kilometa zisizopungua kama kilometa 100. Ndiyo maana katika jibu letu la msingi tumesema tumeona tumefanya tathmini, kuvunja ule mlima ni gharama sana.

Kwa hiyo, kuna haja ya kutafuta fedha kubwa ili katika huo mradi tuweze kupindisha barabara kuzunguka hiyo milima ili tuweze kuwa na uhakika wa kuipitisha hiyo barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi lake limechukuliwa, lakini ni wazi kwamba fedha inayohitajika ni eneo la zaidi ya kilometa 100. Kwa hiyo, ni bora tukaamua kabisa kuujenga huo mradi. Hata hivyo, bado tumeendelea kutoa fedha kidogo ili kufungua kulingana na fedha inavyopatikana kuunganisha Mkoa wa Ruvuma na Morogoro kati ya Wilaya hizo mbili za Malinyi na Namtumbo. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali iligharamia barabara hii fedha nyingi sana; imejenga madaraja ya Mto Kilombero kwa gharama kubwa, imejenga Mto Furua, Mto Mwatisi, Mto Londo na Mto Luhila kwa upande wa Mkoa wa Ruvuma Jimbo la Namtumbo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haioni sasa ipo haja kukifungua hiki kipande ili tuweze kupita angalau barabara iwe inapitika na gharama zilizoingia kwa Serikali kujenga haya madaraja, basi zionekane zina faida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana nimpongeze Mheshimiwa Vita Kawawa kwa kutambua juhudi kubwa ambazo zinaendelea na Serikali hii ya Awamu ya Tano na ya Sita ambapo tumeshajenga madaraja haya aliyoyataja, dhamira njema ya Serikali ikiwa ni kuiunganisha iwe mkoa. Katika kitu kigumu kwenye barabara ni madaraja. Kwa hiyo, anaeleza pia kwamba Serikali ina dhamira kabisa na ndiyo maana tumeendelea kujenga hizo barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tayari mwaka huu tumetenga shilingi bilioni mbili na nusu kwa ajili ya kuendelea kuijenga hiyo barabara. Kwa hiyo, kadri fedha zitakazopatikana naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kawawa na Mheshimiwa wa Malinyi kwamba Serikali ina nia ya dhati. Kwa hiyo, tutaikamilisha hiyo barabara; na kama walivyosema, inawezekana tukaanzia eneo hilo ambalo sasa limekuwa ni kikwazo zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni lini Serikali itajenga barabara inayoanzia Bunju A kupitia Mabwepande ikiunganisha na Jimbo la Kibamba ambayo barabara hiyo imekaa muda mrefu na ikitolewa ahadi bila utekelezaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Felista Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba yalikuwa pia ni ahadi ya Mheshimiwa Hayati Rais na pia yalikuwa ni maagizo. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba hizo barabara, TANROADS kwa maana ya Mkoa wa Dar es Salaam kusaidiana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI (TARURA) tutahakikisha kwamba hizi barabara zinatekelezwa kuanzia kipindi hiki cha mwaka wakati wa utekelezaji wa bajeti ya kuanzia mwaka huu 2021. Ahsante.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nachukua nafasi hii kuipongeza Serikali kwa kutupa zaidi ya kilometa 80 ya barabara ya lami kutoka Tarime Mjini, kuelekea Serengeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba kwa sababu tayari wananchi wakazi wale wa Tarime waliopo pembezoni mwa barabara wameshabomoa nyumba zao kwa ajili ya kulima barabara ile, lakini kuna kipande ambacho kulikuwepo na Mkandarasi ambaye alikuwa anajenga kipande pale Lebu Center kwenda Mugabiri na tayari yule Mkandarasi anaendelea…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Kembaki.

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo najenga hoja ya swali langu.

NAIBU SPIKA: Huna haja ya kujenga hoja, wewe taja barabara unayotaka kuulizia swali.

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mkandarasi yule anaendelea na ujenzi wa kile kipande na tayari wananchi wamebomoa kwamba ile barabara inajengwa upya kutoka hapo mjini kuelekea…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kembaki uliza swali.

MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni hivi ni kwa nini Mkandarasi yule asingepewa sehemu nyingine ajenge badala ya kujenga sehemu ambayo tayari TANROADS watakuja kujenga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Kembaki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Mkandarasi yupo site na anajenga, namwomba Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa nikutane naye kupata maelezo sahihi kwa ajili ya kutatua hiyo changamoto anayosema ili kwa pamoja na Meneja wa TANROADS Mkoa tuone namna ya kuondoa hiyo changamoto. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na ahadi za viongozi wetu Wakuu wa Serikali na ahadi hizi zimekuwa zikitolewa tangu Awamu ya Nne, Awamu ya Tano na sasa Awamu ya Sita na ahadi hizo zimekuwa hazipo katika mkakati mzuri wa kuziratibu na pengine kuweka bajeti kwa ajili ya kuzitekeleza: Nini mpango mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kwamba sasa ahadi zile zote zinaratibiwa nchi nzima na kuwekewa mkakati wa kibajeti ili mradi ahadi hizi ziwe ni ahadi zinazotekelezeka? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Butondo, Mbunge wa Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Boniphace Butondo kwamba ahadi zote zinazotolewa na viongozi wa kitaifa zimeratibiwa na kwa kweli tunazifahamu na ndiyo maana tunakuwa tunazitambua kwamba zinatakiwa zitekelezwe. Zikishatolewa ahadi zinakuwa ni kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mbunge kwamba kinachogomba hapa wakati fulani huwa ni bajeti kwamba unapanga, lakini hutegemea na bajeti ya Serikali. Kwa hiyo, ahadi zote ambazo zimetolewa zikiwepo na ahadi ambazo zimetolewa katika Jimbo lake, tunazifahamu na tumeziratibu na nyingine tumezipangia bajeti.

Kwa hiyo, ndiyo maana tunasema kulingana na upatikanaji wa fedha zikipatikana, miradi yote ambayo Waheshimiwa Viongozi wetu wa Kitaifa wamezitoa tutaitekeleza. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

(a) Kwa kuwa majibu mazuri yametolewa na Serikali, kwa umuhimu barabara hizi pamoja na kuondoa msongamano sehemu ya pembezoni mwa Mkoa wa Dar es Salaam lakini pia zinasaidia kufungua uchumi wa wananchi wa pembezoni. Aidha, barabara hizi zilipata baraka za Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na kuzitamani zijengwe kwa haraka na udharura. (Makofi)

Je, Serikali sasa haioni inayo kila sababu kukamilisha barabara hizi katika mwaka wa fedha 2022/2023? (Makofi)

(b) Kwa kuwa kilomita zilizotajwa 33.7 ina sehemu ya kilometa 1 ya barabara ya njiapanda ya shule na wanahitaji fidia. Je, Serikali imejipanga vipi kulipa fidia wananchi hawa? (Makofi)
MHE. NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu Mbunge wa Kibamba kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika ni kweli kwamba Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyekuwa Rais aliahidi kwamba, barabara za Jimbo la Kibamba angetamani zijengwe zote kwa kiwango cha lami. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi za viongozi wa Kitaifa, zote tunazichukulia kwa umuhimu mkubwa sana na ndio maana hata akienda kwenye kitabu chetu cha bajeti, tumetenga tayari fedha, kwa ajili ya kuanza upembuzi kwa sababu, barabara zote zilizotajwa katika Jimbo lake ni za vumbi. Kwa hiyo, lazima hatuwezi tukaruka hatua ni lazima tutafanya upembuzi yakinifu na usanifu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge awe na uhakika kwamba tunatambua pia tutafungua uchumi wa Jimbo lakini pia kurahisisha mawasiliano.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwa kawaida barabara zote zinapojengwa tutahakikisha kwamba hiyo fidia aliyoitaja, tunailipa kabla ya ujenzi na kama kuna changamoto zaidi ya hii ambayo tunafahamu ya kuilipa kwa kawaida, basi nimuombe Mheshimiwa Mbunge tuweze kuonana naye kwa ajili ya kupata maelezo zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Barabara ya Murongo kuja Kibale kuja Bugara halafu mpaka Mgakorongo ni barabara ya hadhi ya Mkoa. Ikiunganisha Uganda na Tanzania na mchakato wake umechukua muda mrefu. Nataka kujua ni lini hiyo barabara itaanza kujengwa kwa sababu, imekuwepo mchakato wake muda mrefu. Nataka kujua Serikali imejipangaje? (Makofi)
MHE. NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara iliyotajwa ni barabara kuu na ni barabara ambayo ni kweli inaunganisha Tanzania na Uganda katika lile eneo linaloitwa Murongo. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge barabara ile nimeitembelea na barabara hiyo kwa mwaka huu, imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza kwa kiwango cha lami ujenzi huo. Kwa hiyo, nimuhakikishie kwamba ipo kwenye mchakato na barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kutokana na umuhimu wa barabara inayotoka Mtwara mjini kuelekea Msimbati, ambako kuna visima na mitambo ya gesi. Je, ni lini sasa Serikali itaona umuhimu wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
MHE. NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shamsia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyotaja ni barabara muhimu kwa sababu inaenda kwenye maeneo ya kimkakati. Naomba nimuhakikishie kwamba kadri fedha itakavyopatikana katika bajeti zinapokuja, barabara hii tutaijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, tunaifahamu ni barabara muhimu kutegemea na upatikanaji wa fedha na hasa kwa bajeti ambayo tutaanza kuitengeneza mwezi wa tatu mwakani. Ahsante. (Makofi)
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri na Serikali kwa majibu mazuri yenye kutia matumaini ya wakazi wa Jimbo la Kibiti. Hususani walio jirani na barabara ya Bungu Nyamisati kwa kuwa Serikali imetenga fedha, ya kuanza upembuzi yakinifu na hizi milioni 700 kwa ajili ya matengenezo ili ipitike muda wote.

Mheshimiwa Spika naomba sasa niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa katika hilo Jimbo la Kibiti kuna barabara muhimu ya Kibiti Dimani Mloka ambapo pia, magari yanayoelekea kwenye mradi muhimu wa kimkakati wa ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere wanaitumia.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza upembuzi yakinifu kwa kuwa barabara hii pia ipo kwenye ilani ya uchaguzi ya mwaka 2025, kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami? Ili kuwezesha ipitike muda wote kuelekea kwenye Mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Subira Mgalu Mbunge wa Viti Maalum Pwani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara aliyotaja ni kati ya barabara ambazo zinafika kwenye mradi wetu wa kimkakati na imeainishwa kwenye ilani ya Chama cha Mapinduzi kama alivyosema ambayo ni ya 2020 – 2025. Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara zote ambazo zimeainishwa katika ilani haziwezi zote zikatekelezwa kwa mwaka mmoja. Lakini nimuhakikishie kwamba zipo kwenye mpango na zitafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, kama ilivyoainishwa kwenye ilani katika kipindi hiki cha miaka mitano. Ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nashukuru majibu ya Mheshimiwa Waziri kidogo yanaleta matumaini kwa mbali, lakini kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne japo haijawahi kuwekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi; lakini kwa kuwa TANROADS kila mwaka inapoteza mabilioni ya fedha, kwa mfano mwaka huu barabara hii imetengewa shilingi bilioni mbili, lakini vifusi vipowekwa baada ya mvua kunyesha usiku mmoja tu, kifusi hiki kinazolewa na maji ya mvua na wananchi wa milimani ambapo ni asilimia zaidi ya 65 ya wakaazi wa Wilaya ya Same wanakosa mawasiliano na pia Serikali inaingia hasara: -

Je, upembuzi yakinifu wa barabara hii utafanyika lini ili Serikali isipoteze mapato lakini wananchi wa Mwembe, Mbaga, Bonja mpaka Mamba waweze kupata mawasiliano pale mvua zinaponyesha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Tunafahamu kwamba Sera ya Serikali ni kuunganisha mikoa kwa mikoa na Wilaya kwa Wilaya; vile vile nchi hii na Wilaya hizi za nchi hii kuna tofauti ya mazingira, kwa mfano Wilaya ya Same kuna malima mingi sana, Lushoto kuna milima mingi; Mbinga kuna milima; Kagera na maeneo ya Arusha kuna milima mingi sana: Sasa kwa nini Serikali isichukue ikafanya upembuzi yakinifu wa barabara zote za milimani kusudi wananchi wa milimani waweze kupata usafiri wakati mvua zinanyesha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwenye maeneo ya miinuko vifusi huwa vinasombwa na maji. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna barabara za lami na za changarawe na za udongo. Azma ya Serikali ni kuwa na barabara zote za lami, lakini uwezo huo bado hatujakuwa nao na kwa hiyo Serikali inatengeneza barabara kwa kiwango cha lami, kila mwaka tunatenga fedha ili barabara hizo ziweze kutumika.

Mheshimiwa Spika, bajeti aliyoisema ya bilioni mbili siyo tu kuweka kifusi, ni pamoja na kutengeneza mifereji, madaraja pamoja na makalavati ili barabara hiyo iweze kutumika kwa mwaka mzima. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama alivyosema, tunatafuta fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na hatimae usanifu wa kina.

Mheshimiwa Spika, pengine nitoe maagizo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro aweze kuainisha yale maeneo yote korofi na yenye miinuko mikali ili tuweze kufanyia matengenezo surface dressing ama hata kujenga barabara hizo kwa zege kama ilivyofanyika maeneo mengine kama Mikoa ya Manyara, Ruvuma, Kigoma, ukienda Morogoro; maeneo ambayo ni korofi basi barabara zinajengwa kwa kiwango hicho.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu mikoa, ni kwamba kama tulivyoainisha kwamba tunaunganisha mikoa na mikoa kwa kiwango cha lami, hiyo ndiyo sera ambayo tunayo, lakini wazo la maeneo kwenye miinuko, basi tulichukue na tukiona kama fedha itatosha, basi Serikali itafanya hivyo. Azma ni kuhakikisha kwamba barabara zote zinajengwa kwa kiwango cha lami bila ya kujali eneo eneo na eneo. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika nashukuru kwa kupata nafasi. Kwanza nianze kwa kuipongeza Serikali kwa kutumia pesa nyingi sana kujenga Daraja la Yangoma ambalo lilikuwa ni kero kubwa sana kwa wananchi waliopo kwenye barabara hii. (Makofi)

Mheshimwia Spika, kulingana na ubora wa Daraja la Yongoma lililojengwa ambalo Naibu Waziri, Mheshimiwa Waitara, alikuja tukaenda kuliona. Kweli Serikali hamwoni kuna umuhimu wa kuijenga ile barabara iwe na hadhi sawa na lile daraja lililowekwa pale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru kwa kupongeza kazi nzuri ambayo imefanyika ya kujenga lile daraja. Pili, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kujenga daraja hilo maana yake ni maandalizi ya kuja kujenga pia barabara nzuri inayofanana na hilo kwa sababu hatutajenga tena.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana kwenye jibu letu la msingi tumesema tunatafuta fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili sasa hiyo barabara iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Hiyo hatua hatuwezi kuiruka, ni lazima tuifanye na ndiyo maana tunatafuta hiyo fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Ili Bandari ya Mtwara iweze kufanya kazi kwa ufanisi na kuweza kushughulikia mzigo mkubwa inategemea ujenzi wa reli kutoka Mtwara hadi Mbambabay.

Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusu radi huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, baada ya upanuzi mkubwa wa Bandari ya Mtwara, bandari hii sasa inakabiliwa na changamoto ya vitendea kazi vya kisasa:

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka vitendea kazi vya kisasa katika Bandari yetu ya Mtwara?
NAIBU WAZIRI YA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Chikota kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Mbunge anataka kujua mpango wa Serikali kujenga reli ya kutoka Mtwara kwenda Mbambabay; huu mpango ndiyo unaosimamiwa na watu wa TPA wanaufanyia kazi. Tunajua umuhimu wa eneo hilo, Mheshimiwa Mbunge atupe muda, hili jambo tukalifanyia kazi mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anataka kujua kama kuna mpango wa kununua vitendea kazi. Mpango mkakati sasa wa TPA wa kuweza kuboresha bandari zetu na hasa eneo la Mtwara, ni mpango ambao upo katika mpango kabambe wa awamu ya pili na fedha zinaendelea kutafutwa na tumeshawaelekeza watu wa TPA waje na mpango mkakati wa maandishi twende kuboresha maeneo haya na bandari zote muhimu kimkakati kutokana na kupatikana fedha.

Mheshimiwa Mbunge tunaendeleza ushirikiano, jambo hili limepokelewa na Serikali na Kamati ya Bunge ya Bajeti imetoa maelekezo, vile vile na Kamati ya Miundombinu na tumelipa uzito unaostahili.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ABEID I. RAMADHANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri yenye natumaini ya Serikali lakini naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Mheshimiwa Waziri anatuambia kwamba mkataba umeshasainiwa tangu Oktoba, 2021 ambapo utachukua mwaka mzima mpaka 2022 mwishoni. Kwa nini sasa upembuzi yakinifu uchukue muda mrefu hivyo kwa kilomita 93 tu wakati tayari fedha zipo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Kwa kuwa hadi sasa sijaona chochote kinachoendelea katika barabara hii, Waziri yuko tayari kuongozana nami hadi site kwenda kuona na kusimamia utekelezaji wa kazi hii uanze ipasavyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhan, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kilomita 93.3 ni kilomita nyingi na tunachofanya siyo tu upembuzi yakinifu ni upembezi yakinifu na usanifu wa kina ambao ndiyo utatoa sasa gharama ya hii barabara itahitaji kiasi gani. Kwa hiyo, baada ya hilo nadhani pengine kwa bajeti itakayofata ndiyo sasa tutakuwa tumepata gharama ili kuanza kuingiza kwenye mpango kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge ambao barabara hii inawahusu, mara baada ya kikao hiki cha Bunge nitatembelea Mkoa wa Singida kwani natambua barabara hii inaunganisha Singida, Manyara hadi Simiyu.

Kwa hiyo, nimejipanga kutembelea hii barabara, Mheshimiwa Mbunge awe tayari kwamba tutaongozana kuangalia hii barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kupitia bajeti ya mwaka huu wa fedha (2021/2022), Serikali imepamga kujenga barabara kwa kiwango cha lami Morogoro - Njombe Boda walau kwa kuanza na kilomita 50. Swali langu: Je, ni lini Serikali itatangaza zabuni walau ujenzi huu uanze kwa kilomita 50 hizi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Kunambi, Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge nataka nikuhakikishie kwamba barabara zote ambazo zimetengewa fedha tayari ziko kwenye michakato ya manunuzi. Kwa hiyo, mara tu hizo hatua zitakapokamilika, nikuhakikishie kwamba zitatangazwa kwa ajili ya kuanza ujenzi. Ahsante.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nilitaka kuuliza swali la nyongeza kwa Wizara ya Ujenzi kwamba katika kazi zilizotangazwa na zilizoanza kufanyika sasa hivi na TANROAD kule Kigoma, nyingi zimekwama kwa sababu GN hazijatolewa. Je, mna mpango gani wa kufanya mawasiliano na Wizara ya Fedha kuhakikisha GN hizo zinatoka kabla mvua nyingi hazijaanza kunyesha katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inafanya mawasiliano na Wizara ya Fedha na tunapoongea hivi nina hakika muda siyo mrefu GN zitakuwa zimetoka ili tuweze kuanza kutekeleza hiyo miradi haraka kabla ya mvua haijakolea. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, labda kama kuna barabara ambayo ni specific ama kuna shida, hiyo haitatoka GN mpaka wajiridhishe kwamba kila kitu kimekaa sawa. Ila kwa barabara nyingine nina hakika siyo muda mrefu zabuni zote zitatangazwa baada ya kutoka hiyo GN. Ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani na wewe mwenyewe ni shahidi, usanifu umefanyika toka mwaka 2017 mpaka leo tunakwenda miaka mitano, sita bado Serikali inatafuta fedha ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Hivi kweli Serikali mko serious na ujenzi wa barabara hii? Mheshimiwa Flatei alitaka mpaka kupanda juu ya meza, hivi mnawaambia nini wananchi wa maeneo haya, Serikali mna mpango wa kujenga barabara hii lini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili Mheshimiwa Waziri wananchi wa Maswa Mjini wanahitaji taa za barabarani kwa mujibu wa maelekezo yako Mheshimiwa Naibu Waziri taa 60 mmetuwekea taa 18 tu mwaka jana, mna mpango gani wa kumalizia taa zilizobaki katika mji wa Maswa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stanslaus Haroon Nyongo Mbunge wa Maswa Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali iko serious kuijenga barabara hii ambayo nimeitaja inayoanzia Lalago, Mwanuzi, Hydom, Mbulu hadi Karatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ninaomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika eneo la Mwanuzi-Sibiti kwenye bajeti hii tumetenga kuanza na ujenzi na zimetengwa billion 5 na tumetoa kibali lianze kwanza kujengwa daraja linaloitwa Itembe. Lakini katika barabara hiyo ambayo ni muendelezo kipande cha Mbulu Hydom tayari tumeshatangaza barabara kilomita 23 na tunaomba kipande chote kile kitangazwe, kwa hiyo muda wowote tutatangaza kilomita zote 50 ikiwa ni muendelezo wa hiyo barabara kuhakikisha kwamba yote inakamilika. Kwa hiyo, Serikali iko serious na ndio maana kazi zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili naomba nimuhakikishie kwamba tuliahidi tutakamilisha hizo taa 60 na nitoe wito ama nitoe maagizo kwa Meneja wa Mkoa wa Simiyu kuhakikisha kwamba zoezi hili linakamilika kama tulivyoahidi kama Serikali, ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Serikali imewekeza Bandari ya Kabo kwenye Wilaya ya Nkansi lakini changamoto kubwa ambayo inawafanya watu wasitumie bandari ile ni kwa sababu ya kukosa barabara ya kiwango cha lami cha kutoka Lyazumbi mpaka Kabwe na hiyo ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Ningependa kujua ni lini mtajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali imewekeza kujenga Bandari kubwa ya Kabwe ili tuweze kufungua Mkoa wa Rukwa na Tanzania kwa ujumla kufanya biashara na DRC Congo, na ndio maana tumejenga bandari mpya kabisa ya Kabwe. Lakini baada ya kujenga tunajua lazima kuwe na barabara, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi ya kwanza barabara ilikuwa ni finyu.

Mheshimiwa Mweyekiti, kwa hiyo kazi ya kwanza ni kuipanua ile barabara madaraja tunayabadilisha yote na barabara tunaipanua na magari yote yaweze kupitika. Na baada ya hapo sasa mpango unaofuata ni kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami lakini awamu ya kwanza ni kuipanua kubadilisha madaraja ili magari makubwa yaweze kupita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Barabara ya Aliyazumbi Kabwe kama alivyoahidiwa na Mheshimiwa Waziri Mkuu itajengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imetangaza kilometa 25 nashukuru. Je, bajeti ya sasa ina kilometa 50 ni lini sasa utatangaza kilometa 50 ili kufikia Hospitali ya Hydom barabara ile kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay Mbunge wa Mbulu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie kwamba kipande cha kilomita 50 kati ya Hydom na Mbulu tumetangaza kilomita 25 na Wizara tayari imepeleka maombi maalum ili kipande chote kile kiweze kutangazwa na loti nzima ikamilike kwa hiyo tuko kenye hatua nzuri, ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza. Kuna wakati fulani sisi wakazi wa Mikoa ya Kusini hasa Mtwara huwa tunafikiri kama huwa hatuonekani na Wizara hii ya Ujenzi, na ninasema hivyo kwa sababu kuna barabara inayotoka Mtwara, Nivata, Newala, Masasi ikipitia Kata za Chikunja, Lukuledi kuelekea Ndomoni Nachingwea mpaka Liweke ilitengewa kipande hichi cha Masasi Nachingwea kilitengewa kiasi cha shilingi billioni 1.5 tu, na tulimuuliza Waziri kwamba anategemea kuanza wapi katika hili alijibu lakini hakuwa wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninataka kufahamu kipindi cha mvua kinakaribia kuanza sasa hivi na baadhi ya maeneo mvua zimeanza kunyesha na barabara hii wakati wa mvua huwa ni usumbufu mkubwa huwezi kufika Newala kirahisi hauwezi kufika Nachingwea kirahisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ilitenga shilingi billioni 1.5 sasa sisi tunataka kufahamu ni lini hasa na Serikali ituambie kinaga ubaga barabara hii inakwenda kutengenezwa na kukamilika sio maneno maneno yanayotokea sasa hivi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwahakikishie Wabunge wa Mtwara, Newala, Masasi na Ndanda kwamba barabara hii ya kilomita 210 ya kuanzia Mtwara Nivata, Ndanda, Newala hadi Masasi tumeshajenga kilomita 50 bado kilomita 160. Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko kwenye asilimia zaidi 85 na Benki ya Maendeleo ya Afrika iko tayari kuijenga hii barabara na tunauhakika kufikia mwishoni mwa mwezi wa 11 huu tutakuwa tumekamilisha mazungumzo na tunauhakika kwamba wako tayari kuijenga hii barabara. Na kipande hiki cha Masasi kwenda Nachingwea tayari tumeshatenga billion 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali ya Awamu ya Sita haibabaishi ipo serious na kazi hii itafanyika ahsante. (Makofi)
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana, naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi swali la nyongeza. Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya lami katika Barabara ya Iboni, Bolisa na Gubali katika Jimbo la Kondoa Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ussi Pondeza Mbunge wa Chumbuni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa barabara zile ambazo ziko Kondoa mjini barabara nyingi zinahudumiwa na halmashauri kwa zile barabara ambazo zinahudumiwa na Wakala wa Barabara TANROADS naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajenga kama zilivyoainishwa kwenye mpango na kama ilivyo kwenye bajeti yetu ambavyo tumepanga, ahsante. (Makofi)
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa swali la aina hii limeshaulizwa na Mheshimiwa Shanifu Mansour, Mbunge wa Kwimba na swali la aina hii liliulizwa na Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu. Pia mimi mwenyewe niliwahi kuuliza swali la nyongeza kwenye swali la aina hii. Serikali kupitia Mheshimiwa Naibu Waziri aliyetoa majibu leo, ilitoa majibu tofauti na iliyoyatoa leo kwa sababu, ilisema imeshatenga pesa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kilometa 10 katika mwaka huu wa bajeti na katika bajeti hiyo ilionekana. Sasa nataka kuuliza swali na kufahamu, je, Serikali katika ujenzi wa barabara hii inafahamu ni nini inahitaji kuwajibu watu wa Kwimba na Sumve au tunajibu tu ili muda uishe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; barabara hii imeshafanyiwa usanifu, kama majibu ya Serikali yalivyotolewa na kwa mujibu wa usanifu barabara hii, barabara mpya iliyosanifiwa itapita sehemu tofauti na inapopita barabara ya sasa katika eneo la Nkalalo ambapo kuna ujenzi wa reli ya SGR. Kwa sababu kwa mujibu wa ujenzi wa reli hii, hakuna barabara inaruhusiwa inaruhusiwa kupita juu ya reli. Ina maana reli hii ikimalizika kujengwa njia ya kutokea Kwimba kwenda Magu itakuwa imefungwa. Je, Serikali haioni kuna udharura wa kuanza ujenzi wa barabara hii ili kurahisisha usafiri wa watu na mizigo kutokea Kwimba kwenda Magu na kuiunganisha Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba na Mkoa wa Mwanza kwa barabara ya lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Emmanuel Mageni Kasalali, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli katika bajeti tuliyopitisha na bado sijaiondoa, tulitenga bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Katika jibu la msingi nimesema Serikali inaendelea kutafuta fedha na fedha ndio hii kwamba, tutakapopata sasa tutakuwa tunaanza ujenzi kwa sababu, hatujaanza, lakini ipo kwenye mpango na bado mpango huo haujafutwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hakuna majibu tofauti, majibu ni hayo na ndio bajeti tuliyopitisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, huu udharura anaousema Mheshimiwa Mbunge, naomba nimhakikishie kwamba, kama Wizara tunalichukua na wataalam watakwenda kufanya tathmini na kuangalia kama kinachosemwa kina ukweli, basi tutachukua ushauri na kulifanyia kazi kama kutakuwa na udharura huo. Ahsante.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumwambia Naibu Waziri kwamba tulishapeleka maombi na Serikali ilituma wataalam wakafanya survey mwaka 2013/2014, lakini pia na mwaka 2016 walikuja wakafanya survey wakawa wamewasilisha Wizarani.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia barabara hii ndiyo kiunganishi cha Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Simiyu ambao kimamlaka ulitengenezwa mwaka 2012.

Kwa hiyo, namwomba Waziri aweze kulipa kipaumbele, walifikirie ombi letu na waweze kuipandishwa hadhi ijengwe kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kupokea ushauri wa Mheshimiwa Nicholaus George Ngassa, kama alivyoomba.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie kwamba kama limeshafika Wizarani, basi tutaliangalia tuone kama limekwama; na kama kuna vigezo ambavyo vinashindikana, basi nitaomba tuwasiliane naye ili kama kuna shida tuone. Kama inakidhi vigezo vyote, nadhani barabara hii itapandishwa hadhi. Ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Barabara inayotoka Geita kwenda Nkome ina kilometa 57 na ilishafanyiwa upembuzi yakinifu muda mrefu na ikawekwa mpaka beacon na alama za kuanza mkandarasi. Leo tunazungumza ni karibia mwaka wa pili, tunaahidiwa kila siku: Ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja kuuona Mji wa Nzera ambao ndiyo Makao Makuu ya Halmashauri ya Mji wa Geita; haijawahi kuona lami; kila mwaka tunaahidiwa na leo ni mwaka wa nne?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Barabara ya Kamanga – Sengerema – Buchosa – Nkome ni barabara ambayo imeng’oa Wabunge zaidi ya sita, upande wa Sengerema na upande wa Buchosa; lakini tumekuwa tukipata ahadi zilezile za Serikali kwamba mwakani tunajenga, mwakani tunajenga; sasa nataka kumwuliza Mheshimiwa Waziri, tufundishe njia ambayo unaona ni nzuri na sisi tupite kama ni dirishani angalu tupate hiyo lami. Bado tunapenda kuendelea kuwa Wabunge.

Naomba commitment ya Serikali, ni lini mtaanza kutengeneza Barabara ya Kamanga – Sengerema – Buchosa – Nkome?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.
GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, beacon zilizowekwa haikuwa usanifu wa kina; na fedha iliyotengwa kwenye bajeti ya mwaka huu tunaoutekeleza inakwenda kufanya kazi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, yako maandalizi ambayo yanaendelea kwa ajili ya kuanza huo mchakato wa kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina yakiwa ni maandalizi ya kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya pili aliyoisema ya Kamanga – Sengerema – Buchosa hadi Nkome, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba itatekelezwa kama ilivyoahidiwa kwenye Mpango wetu na kama ilivyoelezwa kwenye Ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka 2020 - 2025. Pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kutafuta fedha na ikipatikana hizi barabara zote zitajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kutokana na umuhimu wa barabara hii Wabunge wengi waliopita upande wa Bahi na upande wa Manyoni, wamekuwa wanaulizia kuhusu umuhimu wa barabara hii na majibu ya Serikali yamekuwa ndiyo hayo, kwamba, tunatafuta fedha kwa ajili ya usanifu yakinifu na ile nyingine aliyoisema.

Mheshimiwa Spika, sasa, tena niulize hapo: Je, ni lini fedha ya upembuzi yakinifu itapatikana? Maana yake ndiyo hayo hayo miaka yote. Sasa ile ya upembuzi yakinifu na ile nyingine, ni lini fedha itapatikana? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwenye majibu ya sehemu (b) nilikuwa naomba Mheshimiwa Naibu Waziri afanye ziara ili aweze kupata uhakika kabisa na alichokijibu hapa. Mimi mwezi wa Nne nilikesha pale, barabara ilijifunga na kinachojibiwa hapa sicho kilichofanyika. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Naibu Waziri baada ya Bunge hili hebu akafanye ziara aweze kuona na mwenyewe awe na picha halisi ya eneo lile.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kenneth Ernest Nollo, Mbunge wa Bahi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni lini? Serikali mwaka huu wa fedha imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza kazi hii. Suala la kutembelea, hilo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, niko tayari kutembelea hilo eneo kwa sababu ni eneo hili hili tu. Nitakapokuwa nakwenda Kaskazini, basi nitapita barabara hiyo na nitamjulisha ili tuweze kukagua pamoja naye hiyo barabara. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa leo ni mwaka wangu wa 12 nikiwa Bungeni, Rais wa Awamu ya Nne alituahidi ujenzi wa barabara ya lami kutoka Kahama, Nyang’hwale mpaka Busisi na Rais wa Awamu ya Tano naye pia aliahidi hivyo, na leo tuko Awamu ya Sita.

Je, Serikali inatuahidi nini ama inatoa kauli gani kuweka fedha kwa ajili ya upembuzi yakinifu kwa ajili ya hiyo barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara zote ambazo zimeahidiwa na viongozi wa Kitaifa zinakuwa zimeratibiwa na zinafanyiwa kazi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara ya Kahama kupita Nyang’hwale hadi Busisi ni kati ya barabara ambazo zipo kwenye Mpango na zitaanza kutekelezwa kadri fedha itakavyopatikana. Labda tuangalie kwa bajeti itakayofuata kama fedha itaruhusu na bajeti itaruhusu, basi tutaiweka kwenye Mpango huo ili iweze kufanyiwa upembuzi na usanifu wa kina. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Barabara ya Bihawana, Chali, Sanza, Manyoni ambayo imeulizwa na Mheshimiwa Nollo ili iweze kukamilika inahitaji ukamilishaji wa ujenzi wa Daraja la Sanza; na kwa taarifa yako upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishakamilika na fidia ilishatolewa kwa wananchi wa Kijiji cha Sanza: -

Je, nini commitment ya Serikali ya lini ujenzi wa daraja la Sanza utaanza? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pius Chaya, Mbunge wa Manyoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli daraja analosema limeshafanyiwa usanifu na litagharimu pamoja na barabara zake za kuingilia shilingi bilioni 23 na barabara zitakazojengwa ni kilomita kama 14.5. Tunavyoongea, tayari tumetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza hiyo kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

(a) Pamoja na mikakati ambayo Serikali imeionyesha je, ni lini sasa ujenzi huo utaanza? (Makofi)

(b) Kwa kuwa Mkoa wa Kigoma una Wilaya tatu mpya ambazo ni Buhigwe, Kakonko na Uvinza. Wilaya hizi hazina viwanja vidogo vya ndege. Serikali ina mkakati gani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kavejuru amekuwa anafuatilia sana suala la ujenzi wa kiwanja hiki, lakini naomba tu nimtoe wasiwasi kwamba kwa maelewano ambayo yanaendelea, tunategemea tarehe 28 mwezi huu wa Pili, kupata Letter of No Objection na miradi yote hii minne tunaamini itaanza kutekelezwa. Hilo ni jibu la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jibu la pili kuhusu ujenzi wa viwanja vya ndege vidogo ama air strip katika Wilaya za Buhigwe, Kakonko na Uvinza, hili litategemea na upatikanaji wa fedha kadri itakavyoruhusu, basi hivyo viwanja vinaweza vikajengwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Kutokana na majibu ya Naibu Waziri ni kwamba tangu mwaka 2018 tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika.

Swali la kwanza, ni lini sasa Serikali itamalizia kuwalipa fidia wale wananchi wa vijiji vya Ikasi, Sanza na Chicheho ambao wanadai takribani shilingi milioni 60 ili kupisha ujenzi wa lile daraja? (Makofi)

Swali la pili ni kwamba, barabara hii ya kutoka Manyoni - Heka - Sanza mpaka Dodoma inaunganisha Halmashauri Nne; Halmashauri ya Itigi, Halmashauri ya Manyoni, Halmashauri ya Bahi na Halmashauri ya Dodoma Mjini. Kwa mantiki hiyo, hii ni barabara muhimu sana kwa sababu inaleta watu kwenye Makao Makuu ya nchi: Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka kuhakikisha kwamba tunatafuta vyanzo vya fedha ili kufungua hii barabara kukuza Mji wa Dodoma? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Daraja la Sanza ambalo litakuwa na urefu wa barabara kilomita 14.5 pande zote mbili limeshafanyiwa usanifu na tunavyoongea hivi, kama Wizara tayari tulishapeleka maombi ya fedha Wizara ya Fedha ili tuweze kuwafidia wananchi wote ambao watapisha ujenzi wa barabara. Baada ya hapo, kama Mheshimiwa Mbunge alivyouliza, tayari tumeshatenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa daraja hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ni muhimu kama alivyosema, lakini haitapitika kama daraja lile halitajengwa. Kwa hiyo, Serikali iliona ni busara kwanza tujenge hilo daraja ili kuwe na mawasiliano ya moja kwa moja mwaka mzima. Ndiyo maana kama nilivyosema, kwa umuhimu huo ambao unaunganisha Halmashauri nne alizozitaja, tunaamini baada ya kukamilika daraja usafiri utakuwa na uhakika na baadaye tutaanza kutafuta fedha kujenga kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Changamoto iliyopo Manyoni Mashariki ni sawa na changamoto iliyopo kwenye Jimbo la Ngara ambapo Serikali ilituahidi miaka 15 iliyopita kutujengea barabara ya Murugarama, Rulenge na Rusahunga kilomita 85 kwa kiwango cha lami. Kwa masikitiko makubwa miaka 15 iliyopita hakuna kilichofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujua sasa: Ni lini; kwa maana ya dakika, saa, siku, mwezi na mwaka ambapo Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi itaanza kujenga barabara yetu kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Naibu Waziri alikuja mwaka 2021, tukaahidi wananchi kwamba barabara hii inaenda kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Naomba niambiwe saa, siku, mwezi na mwaka ambapo barabara hii inaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndasaba, Mbunge wa Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nilitembelea Jimbo la Ngara na moja ya eneo ambalo tulilitembelea ni hii barabara. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ndaisaba, Mbunge wa Ngara, pamoja na wananchi wa Ngara kwamba dhamira ya Serikali bado ni kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba bajeti tunayoendelea kuitekeleza tulitenga fedha. Kwa hiyo, mara fedha itakapopatikana, ujenzi wa barabara hii utaanza kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninashukuru kwa kupewa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kuuliza, barabara ya kutoka Makete kwenda Mbeya takribani kilomita 97 ni barabara ambayo ilipata kibali cha Mheshimiwa Rais katika barabara 16 ambazo tulisomewa kwenye bajeti. Tunamshukuru Mheshimiwa Rais ameongeza kutoka kilomita 25 kwenda kilomita 36.5 za kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami, lakini hadi dakika hii ninapozungumza ni kwamba bado tumebaki kwenye mchakato wa tendering toka mwezi wa Tisa.

Je, ni lini mchakato wa tenda utakuwa umeisha na barabara hii iweze kuanza kujengwa kwa sababu hili ndilo geti la uchumi kwa Wilaya ya Makete lakini pia kwa Mkoa wa Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru kwa kuipongeza Serikali na kwamba barabara yake ni kati ya barabara zilizopata vibali. Hata hivyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Sanga Mbunge wa Makete, kwa kuwa barabara ilishapata kibali cha Mheshimiwa Rais kwamba iendelee kujengwa, taratibu za manunuzi haziwezi zikakiukwa. Kwa hiyo, kama kuna changamoto ambayo ipo, labda Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa naomba tukutane tuone kuna tatizo gani? Ila ni kweli kwamba ikishapata kibali inatakiwa ujenzi uanze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba baada ya kikao hiki tuone kama kuna changamoto yoyote tofauti na taratibu za kawaida ili kama Wizara tuweze kuzitatua. Ahsante. (Makofi)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya Morogoro – Njombe – Boda, umuhimu wake inaunganisha Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini na ni barabara inayotoa alternative, yaani ni barabara mbadala kwa Mikoa ya Mbeya - Iringa - Morogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu dogo la nyongeza ni kwamba, barabara hii ina urefu wa kilomita takribani 222 na kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha zimetengwa fedha ili ujenzi uanze walau kilomita 50; na taarifa nilizonazo, imeshapata kibali: Ni lini sasa Wizara itaanza utekelezaji wa barabara hii? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GEOFREY G. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunambi, Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema, taratibu za manunuzi zinaendelea na mara zitakapopatikana, basi kilomita hizo zitaanza kujengwa. Siwezi nikasema ni lini na tarehe gani, kwa sababu taratibu za manunuzi zina utaratibu wake, zinaweza zikachukua wiki au mwezi. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itaanza kujengwa katika kipindi hiki cha bajeti. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa maswali madogo mazuri ya nyongeza. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini mradi wa barabara inayounganisha Jimbo la Iringa Mjini, Jimbo la Kalenga na Jimbo la Kilolo utakamilika? Kwa sababu mradi huo ni wa siku nyingi sana na wakati wa mvua wananchi wanapata mateso makubwa na barabara hiyo ni ya kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ni lini mradi wa barabara ya Msembe inayokwenda Ruaha National Park utakamilika? Kwa sababu barabara hiyo pia ni ya kiuchumi na inakosesha mapato makubwa sana kwa Serikali kwa kuingiza mapato ya watalii wa ndani na wa nje. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na jibu la barabara ya Ruaha National Park; barabara hii ipo kwenye bajeti na iko kwenye taratibu za manunuzi. Hali kadhalika barabara ya Iringa kwenda Kilolo inaendelea kujengwa na tuna hakika kadri fedha zitakavyopatikana barabara hii ni azma ya Serikali iweze kukamilika kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa inayofanya kwenye miundombinu ya barabara. Tarehe 1 Februari Daraja la Tanzanite limeanza kutumika pale Dar es Salaam. Kwa niaba ya watu wa Dar es Salaam tushukuru sana na nikuombe Kamati za mwezi Machi zifanye ziara Dar es Salaam mpate kupiga picha pale kwenye daraja la kisasa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hali ya barabara kwenye Jimbo la Ukonga inaweza isitofautiane sana na kule Katavi kwa Mheshimiwa Martha aliyeuliza swali la msingi. Iko barabara ya Banana – Kitunda – Kivule – Msongola (kilometa 14.7) ambayo nishukuru sana Serikali imeshajengwa kwa kilometa 3.2 na kwenye Ilani ya Uchaguzi ukurasa wa 78 inaeleza wazi kukamilisha ujenzi wa barabara kwa kilometa 11.5 kutoka eneo la Kivule Mwembeni – Fremu Kumi –Msongola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inahudumia watu wengi na hali yake ni mbaya mpaka inasababisha…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Jerry swali.

MHE. JERRY W. SILAA: …mpaka inasababisha Mbunge siwezi kufanya ziara Kivule bila kuwa na mabaunsa wa kunilinda kutokana na kero kubwa kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa Serikali inieleze, haioni inahitajika jitihada ya dharura kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kwa kilometa hizi 11.5 kama inavyosema kwenye Ilani ya Uchaguzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipokee pongezi kwa niaba ya Serikali kutoka kwa Mbunge kwa kazi ambazo Serikali inaendelea kuzifanya, shughuli za miundombinu na ninaomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Ukonga kwamba barabara ya Banana – Kitunda –Msongola kama ilivyoainishwa kwenye Ilani, lakini pia iko kwenye mpango wa Wizara kujengwa kwa kiwango cha lami na Serikali ina mpango wa kukamilisha barabara hii na ndiyo tayari kwanza tumeshakamilisha kilimeta 3.2 na hizo kilometa zilizobaki tunahakikisha kwamba tutazikamilisha ili wananchi waweze kupata huduma sahihi. Ahsante.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo ya barabara za Katavi yanafanana sana na matatizo ya barabara ya Kawe. Nataka kuuliza swali dogo kwa Mheshimiwa Waziri; barabara ya Bagamoyo – Tegeta imejengwa hapo katikati haina mitaro kabisa na matokeo yake inasababisha mafuriko kwenye maeneo ya Basihaya, DAWASCO na Boko; ni lini sasa Mheshimiwa Waziri utakwenda pamoja na mimi uone jinsi ambavyo TANROADS wamejenga bila mtaro kabisa na inasababisha mafuriko ambayo yanahatarisha maisha ya wananchi? Ni lini Mheshimiwa Waziri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Askofu Gwajima, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie mara baada ya kumalizika kwa Bunge tutaambatana naye kwenda kutembelea barabara hii. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza, lakini pia niipongeze Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kuweka jiwe la msingi barabara ya mwendokasi ya Mbagala, kutoka Bendera Tatu kwenda Mbagala mambo ni mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la nyongeza; ni lini sasa Serikali itakamilisha barabara ya kutoka Mbagala Kokoto mpaka kwenda Kongowe kupunguza msongamano wa magari na kero kubwa ya kupoteza muda katika eneo la Mbagala Rangi Tatu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ni muhimu sana na imeainishwa kukamilishwa kwa kiwango cha lami, lakini itajengwa kulingana na upatikanaji wa fedha na kwa kuwa tuko kwenye kipindi cha bajeti basi tutaangalia ili iweze kupangiwa bajeti kwa mwaka ujao wa fedha. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, ninaomba kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Lupila kuelekea Kipengere ni barabara ambayo inaunganisha Wilaya za Ludewa, Makete na Wanging’ombe na tumeiombea kibali kwenye RCC cha kupandishwa hadhi ya TANROADS, hadi leo takribani miaka mitatu imepita.

Je, ni lini Wizara itatoa kibali barabara iwe chini ya TANROADS ili iweze kujengwa na kupitika kwa uhakika kwa sababu wananchi wangu wanateseka sana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zote ambazo zinahudumiwa na TAMISEMI kwa maana ya TARURA zina utaratibu wake. Naomba kama imefanyiwa tathmini inawezekana imeshindwa kukidhi viwango, lakini tunaomba Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa tuonane ili tuweze kuona ni kitu gani kinakwamisha barabara hii kama inakidhi viwango isiweze kupandishwa hadhi na kuhudumiwa na TANROADS. Ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipokuwa Mbunge wa Kawe, mwaka 2015-2020 barabara ya Chuo cha Ardhi – Makongo Juu – Goba ilikuwa ina changamoto kubwa sana, tukafanikiwa kujenga kipande kutoka Goba mpaka Makongo Juu. Ilivyofika mwaka 2020 kipande cha Makongo Juu kwenda Chuo cha Ardhi akapatikana mkandarasi ambaye ikasemekana angejenga ndani ya mwaka mmoja. Sasa hivi ni mwaka wa tatu toka mwaka 2020 mpaka 2022 mkandarasi aliyeko anasuasua, sasa sijui tatizo ni mkandarasi ama tatizo ni ufuatiliaji.

MWENYEKITI: Uliza swali Mheshimiwa Halima Mdee.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Waziri wa Ujenzi aniambie ni lini kipande cha barabara cha Makongo Juu kwenda Chuo cha Ardhi kitakamilika na kwa viwango vyote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Halima Mdee kwamba barabara hii ambayo inajengwa na anasema inachukua muda nimhakikishie kwamba kutoka hapa nitahakikisha nafuatilia nijue tatizo ni nini na nitatoa majibu kwa nini barabara hii imechukua muda mrefu. Ahsante.
MHE KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. kama ilivyo kwa Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Tanga haujaunganishwa na Mikoa miwili; Morogoro na Manyara. Barabara ya Handeni – Mziha – Turiani na barabara ya Handeni – Kiberashi – Kiteto – Kondoa – Singida; ni lini Serikali itakamilisha taratibu za kuanza ujenzi wa barabara hizi mbili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara inayoanza Handeni kwenda Kiberashi hadi Kwamtoro taratibu zipo zinaendelea kwa kuanza na kilometa 50 na ziko kwenye hatua ya manunuzi; na barabara ya Handeni – Turiani upande wa kwenda Turiani barabara inaendelea kujengwa na bado hatujakamilisha kwa sababu ya upatikanaji wa fedha, lakini tayari nayo tumeshaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, ni matumaini ya Serikali kwamba barabara zote ziko kwenye mpango na zitakamilishwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi, lakini la pili, nikupongeze wewe pamoja na Wabunge wote wapenzi wa Simba Sports Club kwa kuonja ushindi angalau jana; matarajio yetu mtaendelea na utaratibu huo ambao mmeuanzisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu; naomba nipate kauli ya Serikali juu ya matumizi ya barabara wanazozijenga Serikali, hasa barabara ya mwendokasi pale Dar es Salaam na hususan katika Jimbo langu la Kinondoni. Matumizi ya barabara zile yamekuwa mabaya sana, pikipiki zinapita, magari binafsi yanapita, magari ya Serikali yanapita, hali ambayo inasababisha ajali nyingi sana.

Ni nini kauli ya Serikali pamoja na vyombo vyake kuhakikisha kwamba tabia hii ya kutumia vibaya barabara zinazojengwa…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tarimba umeshaeleweka; Mheshimiwa Waziri.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, lakini na la kwanza umenielewa Mheshimiwa, la pongezi. (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimba, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli alichokisema Mheshimiwa Mbunge kwamba kumekuwa na kutokutumia vizuri barabara hizi za mwendokasi na inawezekana ni kwa sababu tu hizi barabara kwetu ni mpya. Lakini naomba nitumie nafasi hii kuwajulisha wananchi wa Tanzania kwamba zile barabara zimewekewa alama na zina matumizi yake. Barabara ya mwendokasi ni ya mwendokasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba nitumie nafasi hii kuhakikisha kwamba watumiaji wote wa barabara hizi za Dar es Salaam ambapo mwendokasi unapita basi wazingatie sheria ili tusisababishe ajali na matatizo mbalimbali kwa watumiaji wa barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Barabara ya Mlowo – Utambalila – Kilyamatundu inaunganisha Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Katavi, na ni barabara ya pili kwa ukubwa ndani ya Mkoa wetu wa Songwe. Kwa sasa hii barabara maeneo ya Itewe pale Itaka pameharibika na imesababisha kero kubwa kwa wananchi wa Songwe, Mbozi na mikoa ya jirani. Ni nini kauli ya Serikali kuhusu matengenezo ya haraka yanayohitajika ili kuinusuru barabara hiyo na hizi mvua zinazoendelea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mlowo – Itaka – Kilyamatundu ni barabara muhimu sana kwa Mkoa wa Songwe ambayo inaunganisha na Mkoa wa Rukwa; na kwa kuwa hiki ni kipindi cha mvua, naomba pia nitumie nafasi hii kuwajulisha na kuwaelekeza Mameneja wote wa TANROADS kuhakikisha kwamba kila kunapotokea changamoto kwenye barabara ambazo tunazihudumia basi wazishughulikie mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Songwe kesho afike eneo la Itaka, Kijiji cha Itewe kwenye changamoto ili aweze kutatua hiyo changamoto, na mimi mwenyewe binafsi na Mheshimiwa Mbunge tuweze kupata majawabu. Ahsante.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Novemba nilikuwa kwenye kata yangu inaitwa Lugulu, Mheshimiwa Naibu Waziri akanifuata kule akaja akaniambia kwamba barabara yangu ya Mkomazi – Kisiwani Same yote inatangazwa kujengwa moja kwa moja.

Sasa ninapenda Mheshimiwa Waziri awatangazie wananchi wangu ndani ya Bunge kile alichoniambia kule Lugulu ili wananchi wangu wasikie. Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru na nimpongeze Mheshimiwa Anne Kilango kwa kufuatilia maendeleo ya barabara za jimbo lake; na ni kweli nilikwenda kwenye jimbo lake na yalikuwa ni maagizo pia ya Kiti kwamba niende nikatembelee barabara za Same.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi zote ambazo tumeziongelea sana ziko kwenye hatua mbalimbali za manunuzi ikiwepo na barabara aliyoitaja ya Kisiwani –Mkomazi. Ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri kweli ya Serikali, lakini je, barabara hii ambayo imengojewa kwa muda mrefu sana na Serikali inaendelea kutafuta fedha. Je, wananchi wa Jimbo langu wasubiri mpaka lini ili barabara hii ianze kujengwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kipande kile cha Mambari – Bukumbi, Shitaga na Ishihimulwa, je, ni lini Serikali itaweka katika bajeti fedha za kufanyia usanifu wa ujenzi wa barabara hii? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge aone jitihada za Serikali, ni mwaka jana tu 2020, tumekamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa maana, ya maandalizi ya kuanza kujenga kwa kiwango cha lami kilomita hizo 56. Hata hivyo, barabara iliyobaki tumekiri kwamba bado haijafanyiwa upembuzi na Serikali inatafuta fedha.

Kwa hiyo, Mheshimiwa avute subira, Serikali ina mpango na ndio maana tayari tumeshaanza hatua na fedha itakapopatikana tutaanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Kipande kilichobaki hadi Muhulidede kitafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi ya ujenzi kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka kujua wananchi wa Kokoto, Mzinga mpaka Kongowe ambao walithaminiwa zaidi ya miaka minne sasa, je, ni lini sasa Serikali itawalipa fidia zao ili ujenzi wa barabara hiyo uanze? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chaurembo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kokoto, Zinga, Kongowe ni kweli inasubiri fidia zifanyike ili barabara ianze ujenzi. Naomba nimhakikishie taratibu zinaendelea na Serikali, ili tukishapata tathmini na kupata fidia kamili tutaanza kuwalipa na utaratibu wa ujenzi wa barabara hii utaanza. Kwa sababu, hatuwezi kuanza ujenzi kabla ya fidia. Ahsante.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami kuunganisha barabara ya Mnivata – Tandahimba – Newala – Masasi kwa kuwa tulishaona kwenye vyombo vya habari upatikanaji wa fedha umekamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agnes kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Agnes kwamba barabara ya Mnivata – Tandahimba- Newala hadi Masasi yenye urefu wa kilomita 210; kilomita 50 Mtwara hadi Mnivata imekamilika na tayari barabara hii ipo kwenye taratibu za manunuzi ambapo itafadhiliwa na Benki ya African Development kwa ajili ya ujenzi wa barabara yote. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri: Je, ni lini Serikali itamalizia barabara ya Bonyokwa – Kimara ambayo tangu mwaka 2021 ilikuwa kwenye bajeti ambayo ni kilomita 3.5? Ni lini itawekwa lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bonnah Kaluwa, Mbunge wa Segerea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoisema ya Bonyokwa ipo kwenye mpango wa TANROADS wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Serikali bado inaendelea kutafuta fedha kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Segerea kwamba hii barabara ni muhimu sana ambayo inaunganisha Segerea na Kimara; na tutaijenga kwa kiwango cha lami mara fedha itakapopatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda kuuliza swali langu la nyongeza kwamba, barabara ya Tarime - Mugumu - Serengeti ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Mkoa wa Mara na Tanzania ukizingatia watalii wanaotokea Kenya kuingia Mkoa wa Mara: -

Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ukizingatia wananchi ambao walikuwa wanaishi kandokando ya barabara hii kwa upande wa Tarime wamebomolewa nyumba zao na waliokuwa wanafanya biashara kuondolewa ili kupisha ujenzi wa barabara hii? Je, ni lini ujenzi utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Tarime hadi Mugumu - Serengeti tayari imeshakamilisha usanifu wa kina na Serikali iko kwenye kutafuta fedha kuijenga; lakini ilionekana ni busara kujenga kwanza daraja ambalo lilikuwa linasumbua sana ambalo tumelikamilisha. Baada ya hapo fedha ikishapatikana tutaanza ujenzi kwa kiwango cha lami.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita nane kati ya kilomita 42 inayoanzia Kibosho Shaini – Kwa Rafael hadi International School?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Partrick Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge ametaka kujua ni lini Serikali itakamilisha kipande cha kilomita Nane cha barabara yake ya kutoka Kibosho Shaini - Kwa Rafael hadi International School. Barabara hii ina urefu wa kilomita Nane. Serikali ilishaanza na ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha na ikipatikana, kipande hiki cha kilomita nane zilizobaki itakijenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, barabara inayotoka Singida kwenda Sepuka kupita Ndago mpaka Kizaga yenye urefu wa kilomita 95 iliahidiwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapunduzi toka mwaka 2015 na Rais Hayati Dkt John Joseph Pombe Magufuli alipokuja kwenye kampeni kwenye Jimbo langu aliahidi kujengwa kwa barabara hiyo kwa kiwango cha lami: -

Je, ni lini Serikali ya Chama cha Mapinduzi itakwenda kutekeleza ahadi hii ikiwa ni moja ya kumbukumbu ya kuenzi ahadi za Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kingu, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya kutoka Sepuka hadi Ndago, kama alivyosema ni ahadi ya Kiongozi wa Kitaifa; na moja ya vipaumbele vya Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatimiza ahadi zote za Mheshimiwa Rais. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itajengwa. Namwaomba Mheshimiwa Mbunge mara baada ya hapa kwa sababu pengine ni kipindi cha bajeti, basi tunaweza tukaonana ili tuone namna ambavyo tunaweza tukaingiza kwenye bajeti zinazoendelea kupangwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali itakamilisha upanuzi wa barabara ya Moshi – Arusha kipande kinachoanzia Tengeru - Moshi mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimo, Mbunge wa Moshi kama ifuatavyo: -

Mhesimiwa Mwenyekiti, huu ni mwendelezo wa barabara ambayo ipo kwenye mpango. Tayari tumeshaanza huko Arusha na tunategemea kwa sababu ni barabara muhimu kutoka Arusha kwenda Holili naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ipo kwenye mpango na tunaendelea. Ninaamini katika bajeti inayokuja barabara hii itapata mwendelezo wa kuijenga hatua kwa hatua kadri fedha inavyopatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. SALIM MUSSA OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Miezi mitatu iliyopita Mheshimiwa Waziri wa Uchukuzi alipokea ndege pale Zanzibar; moja ilikuwa na jina la Tanzanite na nyingine ilikuwa na jina la Zanzibar; na aliahidi kwamba wataongeza miruko hadi Pemba: -

Je, ni lini Wizara hii itasukuma Shirika hili ili kuweza kufika Pemba? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Salim Mussa Omar, Mbunge wa Gando kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekitk, kama Waziri alivyoahidi, ahadi hiyo ipo kwenye utekelezaji. Kwa hiyo, taratibu zote zitakapokamilika, ndege zitaanza kufanya safari kwenda Pemba.Ahsante.
MHE. ALEXANDER P. MNYETI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Barabara hii tunayoizungumzia hapa ni barabara ambayo imekuwa kwenye Ilani ya Uchaguzi kwa mihula mitatu mfululizo, 2010, 2015 mpaka 2020; na Mheshimiwa Rais alipokuja Misungwi aliahidi barabara hii ianze kutengenezwa kwa kiwango cha lami haraka iwezekanavyo na Mheshimiwa Waziri tulikuwa naye pale, maelekezo ya Rais yalitoka hadharani kuwa barabara hii itengenezwe. Sasa anaposema kwamba anatafuta fedha sijajua yeye ni TRA ama ni nini, kwa sababu mwenye TRA ambaye ni Mheshimiwa Rais amesema barabara ianze kutengenezwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza ni kwamba, ni lini Wizara itaanza kujenga barabara hii? Kwa sababu imekuwa ikikarabati vipande vidogo vidogo ambavyo havina tija yoyote kwenye barabara hii. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pastory Mnyeti, Mbunge wa Misungwi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tayari jitihada za Serikali zimeonekana, tumeshafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Pia ili kuhakikisha kwamba barabara hii inatumika tumeshaanza kujenga madaraja ambayo mara nyingi yanafanya barabara hii isipitike.

Mheshimiwa Spika, kwa upande mwingine wa barabara hii tayari tumeshaanza kujenga kilometa tano upande wa Kahama, ambayo ni barabara hiyo hiyo. Kwa hiyo Serikali ina nia njema na mara fedha itakapopatikana yote barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kama ahadi za viongozi wa kitaifa walivyoahidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa ni ahadi ya muda mrefu ya viongozi kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya Mbalizi - Shigamba. Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara imeahidiwa na viongozi mbalimbali wametoa ahadi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara hii ipo kwenye mipango ya kuanza kufanyiwa usanifu wa kina kama maandalizi ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nikushuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Mkutano wa Tatu wa Bunge lako hili niliulizia kuhusiana na Barabara ya kutoka Kiranjeranje, Nanjilinji mpaka Ruangwa kujengwa kwa kiwango cha lami na majibu ya Serikali ilikuwa kwamba itajengwa mara tu fedha zitakapopatikana.

Mheshimiwa Spika, sasa je, Serikali iko tayari kwa mwaka ujao wa 2022/2023 kutenga fedha kwa ajili ya kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, ambayo iko kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama Cha Mapinduzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kiranjeranje hadi Ruangwa ambayo Mheshimiwa Mbunge ameisema, ni kweli ipo kwenye Ilani. Hata hivyo, kama nilivyosema, ni kipindi hiki tunachoendelea na bajeti, barabara hii pengine mwaka huu itakuwepo kwenye mpango kwa ajili ya kuanza maandalizi ya kufanya usanifu wa kina. Ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Changamoto ambayo inawakumba watumiaji wa Bandari ya Kabwe ni barabara inayotoka Lyazumbi kwenda Kabwe na ni agizo la Mheshimiwa Waziri Mkuu. Napenda kujua, ni lini agizo hilo litatekelezeka kwa kuanza kujenga hiyo barabara ili tufikie malengo ya bandari yetu waliyowekeza fedha nyingi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara aliyoisema ya Lyazumbi hadi Kabwe inakwenda kwenye bandari ambayo Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa sana kwa ajili ya biashara kati ya Tanzania na DRC Congo. Naomba nimhakikishie Mbunge kwamba ziko jitihada zinafanyika za kuijenga kwa kiwango cha lami, lakini mpango uliopo sasa hivi ni kipanua ile barabara na kujenga madaraja makubwa na kuiweka kwa kiwango cha changarawe ili magari makubwa yaweze kupita wakati Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya mpango wa kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu yale yale ambayo alinipatia mwaka 2021 leo yamejirudia tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza kwenye swali hili. Kwa vile mazungumzo ya ahadi yaliyotolewa na Barrick yamechukua muda sasa na hayana mafanikio: Nini kauli ya Serikali kwa ujenzi wa barabara hii bila kuhusisha Barrick ili iweze kufanyika? Kwa sababu wale waliotoa ahadi wanaonekana kama hawapo tayari kutekeleza ahadi hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa vile upembuzi yakinifu wa barabara hii umeshafanyika toka mwaka 2017, lakini nasikitika kwamba nyumba zilizoko barabarani zote hazina alama: -

Je, nini mpango wa Serikali kuonyesha wananchi kwamba nyumba hizi zitabomolewa kama barabara itajengwa hivi karibuni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Magessa, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, bado mazungumzo yanaendelea na yako kwenye hatua nzuri. Kama yangekuwa yamekwama, tungeacha na kutafuta utaratibu mwingine. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mazungumzo yanaendelea kati ya Barrick na hizo Wizara ambazo nimezitaja.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tunapoweka alama za kuanza kubomoa, ni pale ambapo taratibu zote za kuanza ujenzi zimeanza na fedha ya kutoa fidia imeshapatikana. Tukishafikia hatua hiyo, basi tutaanza kuweka alama kuonesha wananchi ambao watapisha barabara hiyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza kuhusu barabara ya Ngongo - Milola na Michiga. Hii barabara ina urefu wa kilomita 82. Tuliambiwa itajengwa kwa kiwango cha lami, lakini mpaka leo bado hatujaiona hiyo lami. Kibaya zaidi kwenye barabara hii, sasa hivi mvua hizi zinazonyesha, hii barabaraba imekatika yote na wakaweka mchepuko, diversion ya pili; na hata ile diversion ya pili nayo imekatika; na barabara hii ni kiungo muhimu baina ya Majimbo matatu; Jimbo la Lindi, Jimbo la Mchinga na Jimbo la Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tunaomba kauli ya Serikali, lini barabara hii itarekebishwa? Kama siyo kurekebishwa ina maana kwamba Majimbo haya yote yatakuwa yamejifunga. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI – (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Salma kwa jinsi ambavyo anafuatilia hii barabara ya Ngongo - Milola - Michiga yenye kilometa 82. Barabara hii inapita kwenye miinuko mikali; na kama alivyosema pia kuna maporomoko mengi ya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara hii imekatika, naomba kutumia nafasi hii kumwangiza Meneja wa TANROAD ahakikishe kwamba kesho anafika maeneo yote na kuhakikisha kwamba anapeleka Wakandarasi kwa ajili ya kurekebisha hii barabara na nipate taarifa kuanzia kesho ambapo pia atawasiliana na Mheshimiwa Mbunge kuona kwamba hili suala linafanyika ili kuhakikisha kwamba barabara hii inapitika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi kwa kiwango cha lami, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina azma ya kuijenga na fedha bado zinaendelea kutafutwa. Basi zikipatikana, tunaanza kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.(Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imefanya kazi kubwa sana ya kujenga barabara nzuri kutoka Ndondo mpaka Kigoma. Tatizo kubwa linalotukabili sisi Urambo ni kwamba kona ya kuingilia Urambo Mjini inasababisha ajali kubwa sana. Sasa kwa kuwa nilishaomba Serikalini kujengewa round about na Serikali imeshafanya utafiti wake, imeshapata na gharama: Je, Serikali iko tayari sasa kujenga hiyo round about. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama alivyosema kwamba kama tathmini ilishafanyika, maana yake ni kwamba Serikali ina dhamira ya kuijenga. Naomba baada ya hapa, nimwombe Mheshimiwa Margaret Sitta tuweze kuona ni wapi tumekwama ili tuweze kuamua, kwa sababu kama kazi imeshafanyika, maana yake ni kwamba Serikali imeshaona kuna umuhimu wa kujenga.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Miradi mingi ya Serikali ya barabara ina mwaka kati ya mmoja, kumi na mingine hadi 15 na changamoto kubwa ni kwa sababu tunaahidi barabara nyingi, lakini tuna fedha kidogo, hali inayosababisha tunagawana kilometa moja moja, matokeo yake barabara hazikamiliki, lakini tunatumia fedha nyingi sana kulipa interest kwa wakandarasi kwa sababu hatulipi fedha zote kwa wakati. Sasa Kamati ya bajeti ilishauri kwamba kwa nini Serikali isianze kumaliza barabara zote ambazo ziko kwenye mpango, kisha ndiyo tuanze upya?

Je, wazo hili la Kamati ya Bajeti ambalo Bunge limeridhia kwamba tumalize viporo vyote vikamilike, barabara ikamilike; Serikali imelipuuza ama inalifanyia kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali haiwezi kupuuza ushauri wa Kamati ya Bajeti. Pia nataka nimhakikishie Mheshimiwa Halima Mdee kwamba tunaendelea kuufanyia kazi ushauri wa Kamati ya Bajeti na tutakuja kulileta kama Serikali, tuone namna tutakavyofanya kuhusu kuhamua ni barabara zipi zijengwe na kwa wakati upi?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ambayo yamekuwa ni yale yale kila mwaka, lakini mwaka wa fedha ulioisha, barabara ya Geita - Kahama ilitengewa shilingi bilioni tatu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa nini Wizara isitangaze kumpata mkandarasi na kuanza na fedha hizo zilizotengwa ili kipande hicho kitakachoanza kujengwa kianze kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, fedha iliyotengwa hii ni pamoja na fedha tunayotegemea kuipata kama mazungumzo yatakamilika na wenzetu wa Barrick. Kwa hiyo, mara fedha itakapopatikana, basi kazi hizo zitaanza kwa pamoja. Ahsante. (Makofi)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Naomba niulize kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii inaunganisha mikoa ya nyanda za juu kusini; Mkoa wa Morogoro, Mkoa wa Njombe, Mkoa wa Ruvuma, Mkoa wa Mbeya mpaka Rukwa na inatoa alternative route ya barabara ya Iringa - Morogoro yaani kupitia Kitonga. Sasa katika majibu ya Serikali, ameeleza kwa habari ya kipande cha kutoka Ifakara mpaka Kihansi, kuna kipande cha kutoka Kihansi kwenda Masagati - Madeke mpaka Kibena Junction; kipande hiki, zabuni ya kumtafuta Mkandarasi wa kufanya kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ilitangazwa mwaka wa fedha uliopita, hadi sasa hajapatikana.

Mheshimiwa Spika, swali langu sasa: -

(a) Ni lini sasa Serikali inakwenda kukamilisha kazi hii ya kumpata Mkandarasi huyo?

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa za nchi yetu, Mikoa mingi haijaunganishwa kwa lami; swali langu lingine ni kwamba:-

(b) Ni lini Serikali inakwenda kuunganisha mikoa hii michache ambayo haijaunganishwa kwa lami, ukiwemo Mkoa wa Morogoro?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kunambi Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema, ni lini tunakwenda kuunganisha mikoa yote? Ndiyo kazi inayoendelea. Hata katika jibu la msingi, ndiyo maana hata hii barabara tunaiunganisha kati ya Morogoro na Njombe.

Kwa hiyo, tunaendelea na ni kipaumbele kikubwa sana kwa Serikali kuhakikisha kwamba mikoa hii inaunganishwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Mbunge jitihada unaziona, tayari tunatangaza tender katika kuhakikisha kwamba hizi barabara zinaunganishwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mkandarasi upande pili wa kutoka Lupembe - Madeke kuja Taveta, tender inatangazwa tena baada ya kukosa Mhandisi Mshauri. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba taratibu zinaendelea na Mkandarasi na Mshauri atakapopatikana, ataanza kufanya kazi ya kufanya ufanifu wa barabara hiyo. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa barabara ya kutoka Korandoto kuelekea Meatu iko kwenye Ilani: Je, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Kolandoto ambayo inapita Sibiti kwenda Karatu – Haydom – Mbulu, barabara hii ni ndefu na tuko kwenye mpango wa kuanza kuijenga kipande cha Mbulu kuja Haydom kilomita 50. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge na kipande cha Sibiti tayari daraja limeshajengwa na tutategemea katika bajeti ya mwaka huu na ambayo tunaendelea nayo kuwa na barabara za maingilio zisizopungua kilomita 20 pande zote mbili. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tumeshaanza kutekeleza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwanza, naipongeza Serikali kwa kutujengea daraja nzuri linalotuunganisha Wilaya ya Ludewa pamoja na Mkoa wa Ruvuma. Serikali imefanya kazi kubwa sana: -

Je, lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Njombe – Ludewa – Manda – Itoni?

Mheshimiwa Spika, barabara hii ikikamilika itakuwa na umuhimu mkubwa sana wa kuunganisha Ludewa pamoja na Ruvuma, lakini vile vile watu wa Ruvuma watapita shortcut baada ya kuzunguka...

SPIKA: Mheshimiwa, swali la nyongeza hilo.

MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, vile vile bararabara hii itawezesha mradi wa Liganga na Mchuchuma.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Njombe – Ludewa – Manda ni barabara ambayo tayari Serikali imeanza kuijenga. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Tanzania tuna barabara hii tu kilometa 50 ambayo mkandarasi yuko site tunajenga kilometa 50 barabara nzima kwa kiwango cha zege ambayo inakwenda kuunganisha na hilo daraja, hatuna barabara nyingine Tanzania kama hiyo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nataka nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kuanzia junction pale inapotoka barabara kwenda Songea hapa Itoni kwenda Lusitu, hii barabara tayari tunatangaza zabuni kilometa 50 kwenda kuunganisha pale ambapo tumeanza kujenga barabara ya zege ili hatimaye tuweze kukamilisha barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kule handeni kuna barabara inayotoka Magore - Turiani mpaka Handeni. Barabara hii ina ahadi nyingi za viongozi wa Serikali na vile vile barabara hii inaunganisha Mkoa wa Tanga na Morogoro na ni barabara fupi kwa kuja Jijini Dodoma.

Sasa niulize, ni lini Serikali itamalizia kile kipande cha Turiani - Handeni kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa John Marco Sallu, Mbunge wa Handeni Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia barabara zinazopita katika jimbo lake. Kwa swali alilouliza, nataka nimhakikishie kwamba dhamira ya Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan ni kuifungua Tanzania; na kuifungua Tanzania ni kuhakikisha kwamba miundombinu na hasa barabara zinajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Magole - Turiani hadi Handeni ni sehemu ya barabara inayotoka Korongwe - Handeni - Mzia -Turiani - Magole kwenda Kilosa hadi Mikumi. Barabara hii iko kwenye mpango, kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha, maana imeshajenga Magole hadi Turiani; sasa hivi inatafuta fedha za kujenga Turiani kwenda Handeni.

MHeshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba iko kwenye mpango wetu na hata kwenye vitabu vya bajeti inaonekana hivyo. Kwa hiyo, avute Subira, barabara itakamilishwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa nyakati tofauti hapa Bungeni na pia kwenye ziara za viongozi katika Jimbo langu ikiwemo ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu mwezi Oktoba mwaka 2021, niliiomba Serikali iweze kujenga barabara njia nne kwenda Kipatimu kwa kiwango cha lami ambayo ina urefu wa kilometa 50.

Mheshimiwa Spika, nashukuru Serikali imeanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami katika kipande cha kilometa 1.4 katika eneo la mteremko mkali wa Kilimangoge pamoja na eneo la Kijiji cha Ngorongoro:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia eneo lililobaki la kilometa 48.6? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kumba Ndulani, Mbunge wa Kilwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika ziara hiyo nami nilikuwepo na Mheshimiwa Waziri Mkuu kweli aliahidi kwamba barabara hiyo itajengwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii tumeichukua na tunaiingiza kwenye mpango kwa ajili ya kujenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, pia napokea pongezi kwamba tayari tumeshaanza kujenga hizo kilometa chache. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kadiri Serikali itakavyopata fedha, hizi kilomita 48.6 zilizobaki tutajenga barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Njia Nne hadi Kilwa Kipatimu.
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Barabara ya Kimara - Mavurunza – Kinyerezi ya kilometa saba maarufu kama Kikwete Highway iliahidiwa na Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete mwaka 2010 na ilikuwepo kwenye Ilani za Uchaguzi tatu; mwaka 2010, 2015 na 2020.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua, ni lini ujenzi wa barabara hii utaanza? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo Mbunge wa Ubungo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba moja ya vipaumbele vya Serikali ni ahadi za viongozi na hasa viongozi wa Kitaifa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara aliyoitaja ya Kimara kwenda Kinyerezi ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais tutaijenga kwa kiwango cha lami kadiri fedha zitakavyoendelea kupatikana. Tunajua baada ya kuwa na Stendi ya Magufuli, hii barabara ni muhimu sana kwa sasa kupunguza msongamano kwenye barabara zetu za Mji wa Dar es Salaam. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. TIMETHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya Magokweni - Maramba – Daluni – Mashewa Mpaka Korongwe ni barabara muhimu sana kwa uchumi na ulinzi na usalama wa nchi yetu; na kumekuwa na ahadi za viongozi za muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua, ni lini Serikali itatengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi, baada ya Bunge tulilomaliza hii barabara, nimeitembelea kuanzia Mabokweni mpaka Korogwe na hasa kutokana na umuhimu wa hii barabara.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha. Hata hivyo, kitu tunachokifanya sasa hivi kwa jinsi ilivyopita kwenye miinuko tutaanza kwanza kujenga barabara katika hali zile zenye changamoto ngumu kujenga vipande vifupi vifupi kwa njia ya lami ili njia ipitike kwa muda wote wakati Serikali inatafuta fedha kujenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pia nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Serikali imesema inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara ile kwa kiwango cha lami na kuna maeneo ambayo hivi sasa magari hayapiti yanakaa siku mbili, tatu kufika mwisho wa safari, kama maeneo ya kutoka Mkandu mpaka Mbesa, eneo la Lusewa mpaka kufika Ligunga na eneo la Majiwe mpaka Milonji ambayo yamekuwa ni maeneo korofi kwa muda mrefu. Je, Serikali haioni sasa haja ya kuweka lami laini katika maeneo hayo ili magari yaweze kupita kwa urahisi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa barabara hii haijawahi kukanyagwa na Naibu Waziri wala Waziri wa Ujenzi, naomba anipe commitment ya yeye na mimi kufuatana kwenda kukagua barabara hiyo ili aone adha wanayoipata wananchi katika maeneo hayo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maeneo aliyoyataja ya Lusewa, Mbesa, Malonji nadhani ni jana magari mengi yamekwama. Jana tulitoa maelekezo kwa Mameneja wote wa TARURA Mkoa, naamini watakuwa wananisikia na watakuwa pengine wako site eneo hilo ili waweze kukwamua magari hayo.

Mheshimiwa Spika, hii barabara sasa hivi mwaka huu tumeitengeneza kwa changarawe barabara yote ya kilometa hizi 320. Kwa hiyo nimhakikishie Mbunge kwamba Mhandisi wa Mkoa ninavyosema hivi yuko site kukwamua hayo magari yaliyokwama.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na naamini pamoja na Mheshimiwa wa Namtumbo, kwa sababu barabara hii ndiyo barabara muhimu sana kwa watu wa Tunduru na Namtumbo niombe baada ya hapa tupange ziara tutembelee hiyo barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Jiji la Arusha linakua kwa kasi sana na kusababisha misongamano mbalimbali, kwa hiyo napenda kufahamu; je, ni lini Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi itaanza rasmi ujenzi wa barabara ya lami ya kutoka pale Kiserian (Moshono) kuunga na bypass na ile ya Ngaramtoni kwenda mpaka Mianzini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga hiyo barabara ya kuanzia Moshono kwenda bypass na tayari tumeshaanza, labda ni kuikamilisha tu. Kwa hiyo Serikali bado itaendelea kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa barabara ya pili aliyoitaja ya kuanzia Mianzini kwenda Ngaramtoni yenye urefu wa kilometa 18, ninavyoongea hapa ipo kwenye hatua za manunuzi kuanza kuijenga yote kilometa 18 kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali iko katika mpango wa kutafuta pesa ya kujenga barabara hiyo ya Mtwara Pachani – Tunduru Mjini.

Je, Serikali haioni haja ya kujenga angalau kilometa tano tu za lami ambapo barabara hiyo inapita Tunduru Mjini Na ofisi zote za Serikali pamoja na taasisi za Kiserikali ziko kwenye barabara hiyo ambapo hakuna lami kabisa na zipo mjini kabisa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara nyingi zinazopita katika ofisi zipo ambazo tunazihudumia sisi, lakini pia na TAMISEMI. Tumelichukua hili, tutakutana na wenzetu wa TAMISEMI tuone namna ya kutafuta fedha ili miji hii iweze kupata lami angalau kwa uchache kama miji mingine. Ahsante. (Makofi)
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Barabara ya kutoka Kilindi – Kiteto
– Chemba mpaka Singida ni barabara ya kimkakati ya kuchochea uchumi kwenye mikoa hii minne na wilaya zake. Bajeti hii tunayokwenda kumaliza ilikuwa inaze lakini mpaka sasa michakato yake bado ni mirefu na hatuoni dalili ya kwenda kuanza ujenzi wa barabara hii. Je, ni lini sasa ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami unaanza? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti Yusuph Majala, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoisema ni sehemu ya barabara inayoanzia Kilindi – Kiberashi – Kiteto hadi Kwamtoro, Singida. Naomba nimhakikishie kwamba kama nilivyosema, barabara hii ndiyo inayopita kwenye Bomba la Mafuta la kutoka Tanzania kwenda Uganda. Kwa hiyo Serikali ya Awamu hii ya Sita imejipanga kuhakikisha kwamba kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha barabara hii inaanza kujengwa. Hivi ninavyoongea barabara hii inaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, tuko kwenye hatua za manunuzi kwa barabara hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. JONAS V. ZEELAND: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nichukue nafasi hii niipongeze Serikali kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa changamoto ya barabara iliyopo Mzumbe kwenda Mgeta inafanana kabisa na changamoto ya barabara kutoka Turiani kwenda Mziha mpaka Handeni.

Je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami kutoka Turiani kwenda Mziha hadi Handeni?

Swali la pili, kwa kuwa tuna barabara ambayo ndiyo inasafirisha mazao ya wananchi wetu kutoka Kata ya Kibati, Pemba na Wilaya jirani ya Kilindi.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuiongezea bajeti hii barabara ili iweze kutengenezwa kwa kiwango cha kuridhisha na iweze kupitika nyakati zote, lakini pia na kujenga daraja ambalo ni muhimu sana linalounganisha Wilaya ya Kilindi na Wilaya ya Mvomero katika Kata ya Kibati na Kata ya Kinde? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE.ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee pongeze alizozitoa kwa Serikali kuendelea kufanya kazi katika barabara ambayo ameisema katika swali lake la msingi.

Mheshimiwa Spika, katika barabara aliyoisema ambayo inaanzia Magole – Turiani – Mziha, kipande cha Mziha - Handeni ambacho bado hakijajengwa barabara hii imetengewa bajeti katika mwaka huu wa fedha. Hivyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge awe na subira kadri fedha zitakapopatikana barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ili kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Tanga - Turiani hadi Handeni.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Kibiti ambayo inaenda Kilindi, Tuko kwenye kipindi cha bajeti, ameomba bajeti iongezwe ili tuweze kuijenga kwa kiwango kizuri zaidi. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ombi hilo tumelipokea na tutaangalia namna ya kulifanyia kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne pamoja na Rais wa Awamu ya Tano ya ukamilishaji wa ujenzi wa lami kipande cha Mnata -Mugumu mpaka Arusha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara ya Nata – Mugumu kwenda Arusha ni barabara ambayo inaanzia Makutano- Sanzate – Nata – Mugumu na kuelekea Arusha.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba hadi tunavyoongea mkandarasi yupo site kujenga kilometa 40 kuanzia Sanzate kwenda Nata na baada ya Nata tunafuata Nata kwenda Mugumu. Kwa hiyo, Serikali ina mpango wa kuhakikisha kwamba barabara hiyo inajengwa kwa kiwango cha lami kadri fedha itakavyoendelea kupatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne ambaye aliitoa mwaka 2012 ya kuijenga barabara ya Sangisi - Akeri hadi Ndorombo kwa kiwango cha lami. Ahadi hiyo aliitoa wakati wa mazishi ya aliyekuwa Mbunge wetu Marehemu Jeremiah Sumari? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja na kwa kuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Awamu ya Nne, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tutalichukua kwa uzito mkubwa na ikiwezekana baada ya kipindi hiki cha Bunge tukutane tuone kwa nini imechukua muda mrefu ili tuweze kuona namna ya kutimiza ahadi ya Kiongozi wa Taifa. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara ya Karatu – Mbulu – Hydom – Mkalama – Meatu ni barabara muhimu sana kwa wakazi wa majimbo hayo niliyoyataja.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama ulivyosema barabara hii ya kutoka Karatu – Mbulu – Hydom - Sibiti kuja Lalagwa – Maswa – Kolandoto ni barabara ambayo inaunganisha mikoa mingi, tayari tupo kwenye manunuzi kipande cha Mbulu – Hydom. Pia Daraja la Sibiti kama nilivyojibu kwenye maswali mengine limeshakamilika na tunategemea kuongeza kilometa 20 pande zote kwenye barabara hiyo. Hali kadhalika, kuanzia Kolandoto tupo kwenye mpango wa kutafuta fedha kuanza ujenzi kutokea Kolandoto kwenda Sibiti. Ahsante. (Makofi)
MHE. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Swali la kwanza; kwa kuwa huko nyuma nimewahi kuuliza swali hili humu ndani la barabara hii na daraja hili na nikapewa majibu yanayofanana hivyo huko nyuma zaidi ya mara mbili.

Je, ni lini nitapewa majibu ambayo yanatia moyo zaidi na matumaini zaidi kuliko hayo majibu niliyopewa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa barabara hii inafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kama alivyosema Mheshimiwa Waziri na kazi hiyo inakaribia kukamilika, na kwa kuwa barabara hii na daraja hili linahudumia kata 18 kati ya kata 29 za Jimbo langu, na kwa kuwa hii pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano.

Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa na kukamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini kwa kufuatilia sana hii barabara. Ametaka Serikali impe maneno ya matumaini, naomba niseme siyo tu maneno ya matumaini lakini atakubaliana nami kwamba Wakandarasi sasa hivi wapo site wakiwa wanafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba daraja alilolisema litatekelezwa kwanza kabla halafu wata- submit document lianze kujengwa halafu ndiyo upembuzi na usanifu wa kina wa barabara uendelee wakati daraja hili linajengwa.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Rweikiza awe na imani kwamba kwamba Serikali ya Awamu ya Sita ipo kazini na wananchi wawe na matumaini kwamba walichoahidi Marais kinatekelezwa. Ahsante. (Makofi)
MHE ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza.

Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini ukweli mwenye dhamana ya kutafsiri sheria ni Mahakama na kumekuwepo na kesi ya ardhi chini ya Jaji Bongoyo ya mwaka 2005 ikahukumiwa mwaka 2013. Kesi ya Prochesta Lyimo na wenzake 72 dhidi ya AG na Wizara ya Ujenzi. Katika dhamana hiyo wadai walihalalishwa kwamba eneo ni la kwao na kama Serikali inalihitaji inatakiwa illipe fidia. Swali langu la kwanza, je, ni lini Serikali itatekeleza hukumu hii ya Mahakama?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa, Sheria ya Barabara ya mwaka 1932, Kanuni ya Mwaka 1955 na marekebisho Na. 13 mwaka 2009 inakinzana sana na Sheria nyingine za Mipangomiji na Sheria ya Vijiji ya mwaka 1999 ambayo ilifuta mikataba mingine na sheria nyingine zote zilizotangulia kwa kuweza kuwamilikisha watu ardhi ikiwa ilienda sambamba na zoezi la Operesheni Vijiji ya Mwaka 1974 na 1975 iliyoleta watu pembezoni mwa barabara kubwa na kuwapa miundombinu ya maji na elimu na kadhalika. Je, ni ipi kauli ya Serikali katika mchangamano huu au mchanganyiko wa sheria hizi ya barabara ya mwaka 1932 na hizi nyingine za ardhi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kiamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimfahamishe Mheshimiwa Mbunge wa Kibamba, kwanza nimshukuru na kumpongeza kwa jinsi ambavyo amekuwa akilifuatilia suala hili kila wakati ili kuhakikisha tu wananchi wake hawa wanapata hicho ambacho anawapigania. Naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan inaongozwa kwa mujibu wa Katiba na Sheria iliyopo. Moja ya wajibu wa Serikali ni kulinda wananchi pamoja na mali zake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesi aliyoisema ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ipo kwa Wakili Mkuu wa Serikali ambae yupo chini ya Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Hatua waliyochukua wananchi hawa kupeleka suala hili kwenye vyombo vya kisheria, naomba nimhakikishie kwamba sheria itakapotamka mara ya mwisho nadhani haki itatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili kuhusu sheria kukinzana naomba tu nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara tunatumia Sheria yetu ya Barabara, lakini suala la kukinzana kwa sheria nadhani Serikali imelichukua na itaenda kuangalia sheria mbalimbali zinavyokinzana ili ziweze kusomeka na kueleweka kwa pamoja. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mgogoro wa muda mrefu sana kati ya wananchi wa Kata ya KIA kwa maana ya vijiji saba na Kata ya Rundugai na kule Arumeru dhidi ya Uwanja wa Ndege wa KIA. Mgogoro huu Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba ataumaliza, lakini humu ndani nimekuwa nikiahidiwa na Serikali kila mara kwamba tutaenda kuumaliza. Hivi ninavyozungumza Mheshimiwa Diwani wa Kata ya KIA muda si mrefu amenipigia simu akiniambia kwamba wameanza kuweka alama ya X nyumba za watu bila kushirikisha wananchi na viongozi wa wananchi. Naomba majibu ya Serikali yaliyo thabiti, je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro huu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saasisha Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwa na mgogoro kati ya wananchi na Serikali kwenye uwanja wa KIA. Mbunge amekuwa akilifuatilia mara kwa mara, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi ameshaunda timu ambayo imekwenda kufanya tathmini na kufanya utafiti na mara watakapoleta taarifa tunategemea kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha Mheshimiwa Mbunge atapewa hiyo taarifa na tuna uhakika baadaye tutakwenda kwenye eneo la tukio lenyewe na yeye pamoja na wananchi ili suala hili liweze kufika mwisho. Ahsante. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kwa Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Nanganga, Nangoo, Ndanda, Mwenda, Chikundi, Chigugu, Chikukwe, Chikunja pamoja na Lukuledi ambazo zinapitiwa na barabara kuu inayokwenda Nachingwea kutokea Masasi au barabara kuu inayotoka Mingoyo kulekea Mbamba Bay na Songea. Kwa muda mrefu sasa zaidi ya miaka Kumi hadi Ishirini nyumba za watu pamoja na mali zao zimewekewa alama za X. Ziko alama za X za kijani lakini pia zipo alama za X nyekundu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi hawa wameshindwa kufanya shughuli zao zozote kwa sababu hawaelewi tafsiri ya alama hizi. Nataka kauli ya Serikali itueleweshe ni nini maana ya kuweka alama (X) nyekundu au alama (X) ya kijani kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil Mwambe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, alama hizi zinaonesha kwamba wananchi wamejenga kwenye hifadhi ya barabara ama barabara itapita kwenye maeneo hayo. Wapo ambao barabara imewafuata kijani na wale ambao watatakiwa kufidiwa walikuwepo barabara wamewekewa alama ya (X) lakini ni kwamba hawa wote wataondolewa kwa utaratibu na kwa mujibu wa sheria. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wa Kata ya Kipawa ambao walipisha Airport terminal three tangu mwaka 1997 na sehemu hiyo mpaka sasa hivi shughuli za maendeleo zimesimama. Je, ni lini Serikali itawalipa hawa wananchi fidia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Kamoli, Mbunge wa Segerea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi aliowasema wa Kipawa Airport ambao walipisha ujenzi wa uwanja wa ndege, suala hili nimwombe Mheshimiwa Mbunge aweze kutuletea maelezo sahihi kwa sababu ambao walilipwa na hawa ambao hawakulipwa ili tuweze kujua ni wapi ambao hasa anawasimamia ili tuweze kuwa na majibu sahihi kwa upande wa Serikali. Ahsante.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya kutoka Lushoto, Magamba, Lukozi, Mlalo mpaka Umba Junction ni uti wa mgongo wa shughuli za maendeleo na kujenga uchumi wa wananchi wa eneo hilo. Vilevile barabara hii ipo katika Ilani ya Uchaguzi ya 2015 hadi 2025. Kwa kuwa ipo ahadi ya Serikali ya kuanza kuijenga barabara hii kutoka kilometa moja moja inayofanywa sasa, kwenda katika kuijenga kilometa 10, 10 kila mwaka. Je, ni lini sasa Serikali itaanza utekelezaji wa ahadi hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, imetengwa bajeti kwa ajili ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kutoka mwanzo mpaka kwenye junction ya mwisho ya barabara hii. Je, ni ipi commitment ya Serikali katika kufanya usanifu wa kina na upembuzi yakinifu katika barabara hii ili iweze kuwa mradi kamili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara iko kwenye ilani na ni ahadi ya viongozi, lakini nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Mheshimiwa Shangazi ambaye najua barabara hii inamhusu sana ameshahakikishiwa na Wizara kwamba katika mwaka huu wa fedha, barabara hii itafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na kwa sababu ilikuwa haijafanyika hivyo ndiyo maana ilikuwa ni kusanifu na kujenga. Kwa hiyo tunahakikisha barabara hii itafanyiwa usanifu katika mwaka wa fedha ujao kwa barabara yote. Ahsante.
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kulikuwa na mpango wa ujenzi wa barabara ya Tarime kupitia Nyamwaga, Nyamongo mpaka Serengeti lakini kuna taarifa kuwa mpango huo haupo. Je, ni nini tamko la Serikali juu ya barabara hiyo kwa wananchi wale? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ghati Chomete, Mbunge Viti Maalum, Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni swali lingine tena naulizwa, siku mbili zilizopita liliulizwa swali kwenye barabara hii hii. Naomba nimjibu Mheshimiwa Ghati Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mara kwa kumhakikishia tu kwamba, Mheshimiwa Mwita Waitara, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, jana amekuja ofisini akiwa na madai haya haya, naomba nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo na wananchi wa Tarime, mpango huu unaosemwa hakuna mpango uliofutwa. Nataka nimhakikishie kwamba tayari tuko kwenye hatua za kusaini mkataba kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kuanzia Tarime hadi Nyamwaga, kilometa 25 na zabuni inaandaliwa kuanzia Nyamwaga hadi Mugumu kilometa 61. Jumla kilometa hizo 82, kwa hiyo hakuna mpango uliofutwa na iko kwenye mpango.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Spika. Kwa kuwa changamoto iliyopo kwenye barabara ya Lushoto mpaka Mlalo inafanana na changamoto iliyo kwenye barabara ya kutoka Makofia – Mlandizi mpaka Vikumburu.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kipande hiki cha kutoka Makofia – Bagamoyo mpaka Mlandizi kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alice Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara hii iko kwenye ilani na imetengewa bajeti kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami mwaka huu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ujenzi utaanza mara tu fedha itakapokuwa imepatikana. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukurru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mloo - Kamsamba - Utambalila kupitia Chitete yenye kilometa 145.14 iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020/ 2025 kwenye ukurasa wa 75: -

Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali ilishafanya maandali ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Tayari usanifu wa kina umeshafanyika. Changamoto iliyokuwepo ya Daraja la Momba, imejengwa kwa ajili ya kupokea barabara hiyo. Kwa hiyo, itategemea na fedha zitakapopatikana, kwa sababu taratibu zote za awali zimeshakamilika ili barabara hii ambayo inaunganisha Mkoa wa Songwe, Mkoa wa Rukwa hadi Katavi iweze kujengwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, binafsi naomba kwanza kuipongeza Serikali kwa kuamua kuanza kujenga hata hizo kilometa 20.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, inaunganisha mikoa minne, kwa maana ya Mkoa wa Tanga, Manyara, Dodoma na Singida. Kama hiyo haitoshi, ni kwamba barabara hii ni barabara ambayo Bomba la Mafuta kutoka Hoima Uganda hadi Chongoleani Tanga ndiko linakopita. Sasa nataka kuuliza swali.

Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa haraka na kuhakikisha kwamba kilometa zote 461 zinakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Mheshimiwa Naibu Waziri alifanya ziara ya kupita barabara hii mwaka 2021; na kipindi hiki mvua zinanyesha.

Je, yuko tayari kumwagiza Meneja Barabara Mkoa wa Tanga aweze kufanya marekebisho katika maeneo ambayo yameharibika?Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Kigua pamoja na Waheshimia wote ambao barabara hii inawagusa ambao wamekuwa wanaifuatilia.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wakuu wa Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wameipitisha barabara hii kama ni barabara ya kipaumbele kutokana na umuhimu wake kwa ajili ya bomba la mafuta. Maana linapopita bomba la mafuta ndiyo barabara hii inakopita. Kwa hiyo, Serikali ina mpango kwa kushirikiana na nchi nyingine kutafuta fedha ili ikiwezekana kilometa zote hizi 461 ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la pili, naomba tu kama tulivyotoa agizo kwa wakuu wote wa TANROADS wa Mikoa ahakikishe kwamba anakwenda kwenye madaraja na maeneo yote ambayo yamepata changamoto ya usafiri katika Mkoa wa Tanga; siyo tu kwa Mheshimiwa Kigua, ni pamoja na barabara zake zote ili kuhakikisha kwamba wananchi hawakwami katika kipindi hiki cha mvua. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Mheshimiwa Naibu Waziri mwaka 2021 alifika kwenye Barabara ya Haydom - Katesh na amejionea hali ya ile barabara ambayo inategemewa na wananchi kwa shughuli za kilimo pamoja na huduma mbalimbali: -

Je, ni lini wananchi wa Jimbo la Hanang na Mbulu watawaona wakandarasi wakiwa kwenye kazi kutengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Samweli Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tutafuatilia na kuona kwamba wakandarasi hawa wanakuwepo site haraka inavyowezekana. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa kwenye swali la msingi kulikuwa na hiyo barabara ya Kiberashi na imetengewa Kilometa 25 na tender imeshatangazwa; na Mbulu Vijijini, barabara ya Haydom – Mbulu kulikuwa na tender ya namna hiyo hiyo: -

Je, unataumbaje; tenda hiyo imetangazwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ziko nyingi, ikiwepo moja ya Mheshimiwa Flatei Massay ambayo iko kwenye hatua za mwisho za kusainiwa mikataba ili wakandarasi waanze kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa zoezi la fidia lilianza mwaka, 2012 mpaka 2013 kama sikosei na verification imekuja kufanyika mwaka 2015; na mpaka wananchi kulipwa, wamelipwa mwaka 2021 ambayo ni takribani miaka tisa: -

Je, Serikali haioni haja wale ambao hawakulipwa kwa mujibu wa Sheria yetu ya Barabara ya 2007, ukiwaacha pembeni kulingana na sheria ya awali ya masharti ya ADB kufutwa machozi kwa kuzingatia kwamba wamekaa miaka tisa bila kufanya maendeleo yoyote? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa malalamiko ya kupotezewa muda mwingi wananchi yapo Tanzania nzima kwenye suala zima la kulipwa fidia: -

Je, ni lini Serikali itaileta Sheria ya Barabara ya Mwaka, 2007 Act (No. 13) tukirekebishe kifungu Na. 16 ili kuweze kuongeza muda wa kuwalipa fidia wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eng. Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Tanga. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kuwapigania haki wananchi wa Mkoa wa Tanga ambao anawatetea.

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba katika fidia za wananchi hawa wapo ambao waliridhika na wamechukua fidia, lakini wale ambao hawakuridhika, suala hili walilifikisha Mahakamani. Kwa hiyo, naomba nisiitolee maelezo zaidi.

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu mMarekebisho ya sheria, naomba niseme tumelichukua na tutakwenda kulifanyia kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa barabara ya kutoka Nyigu kwenda Mgololo ambako ndiko kuna kiwanda kikubwa cha karatasi ambao ni uwekezaji mkubwa sana; na ni barabara ya uchumi ambayo imekuwa ikiwasaidia sana wananchi wa eneo hilo: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha barabara hiyo inajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu sana na mbao nyingi tunazoziona zinapita kwenye hii barabara. Naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili amekuja ofisini kama yeye kuliongelea.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hizi ni barabara za kimkakati. Kwa hiyo, namwomba yeye pamoja na wananchi wavute subira kwamba, kulingana na umuhimu wake na jinsi inavyoliingizia Taifa fedha nyingi, basi itakuwepo kwenye mpango ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ujenzi wa barabara ya Mgakorongo kwenda Murongo tathmini imefanyika na wananchi wamekuwa wakisubiri fidia kwa muda mrefu, kiasi kwamba wanashawishika kufanya maendeleo: -

Je, ni lini fidia zitaanza kutoka ili wananchi waweze kuhamia sehemu nyingine waendelee na maisha yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wanaohusika na barabara hii ya kuanzia Omugakarongo, Kigarama hadi Murongo; hii barabara ipo kwenye maandalizi ya kutangazwa zabuni. Barabara hii kabla haijaanzwa tutahakikisha kwamba wananchi hawa kipaumbele ni kuwalipa fidia. Kwa hiyo, kabla hatujaanza kujenga, wananchi kwanza watalipwa fidia na ujenzi wa hiyo barabara utaanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa changamoto wanayoipata wananchi wa maeneo ya Tanga na Pangani ni sawa sawa na matatizo waliyonayo wananchi wa Buchosa ambao ahadi ya Serikali ilikuwa ni kujenga barabara kutoka Sengerema, Nyehunge mpaka Kahunda, lakini wananchi wale wamesimamisha shughuli zao wakisubiri fidia na ujenzi uanze: -

Je, Mheshimiwa Waziri anaweza kuwaambia wananchi wa Buchosa ni lini fidia zitalipwa na lini barabara itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara anayoitaja ya Sengerema – Nyehunge hadi Kahunda yenye kilomita zisizopungua 82 ipo kwenye maandalizi. Kama nilivyosema kwa barabara iliyopita, ni kati ya barabara ambazo zinategemea kuanzwa kujengwa kwa kiwango cha lami kuanzia mwaka huu wa fedha. Kabla ya kuanza ujenzi sheria inatuambia tuwalipe kwanza fidia. Kwa hiyo, mara tutakapoanza kutangaza ujenzi huo, basi na wananchi watapatiwa fidia kwanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante; ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa barabara ya kutoka Mpanda kwenda Karema upembuzi yakinifu unakamilika mwezi wa Aprili na kwa kuwa barabara hiyo ni muhimu, inakwenda kwenye Bandari ya Karema ambako Serikali imewekeza shilingi bilioni 47 na kwa kuwa asilimia 81 ya ujenzi wa bandari imekamilika; na kwa kuwa bandari hiyo...

SPIKA: Mheshimiwa Taska Mbogo uliza swali.

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa bandari hiyo inakwenda kupokea mzigo kutoka nchi za SADC. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba barabara hiyo inajengwa na kukamilika kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa barabara iliyopo sasa hivi ina changamoto kwenye maeneo ya Kaseganyama, Kandilankulukulu na Nkungwi haipitiki kipindi cha masika. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza bajeti ili barabara hiyo ipitike kipindi cha masika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum Katavi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema na kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kutokana na umuhimu wa barabara hii ambavyo kama alivyosema, Serikali imewekeza zaidi ya shilingi bilioni 47 kukamilisha bandari ambayo ipo asilimia 79; ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba hii barabara itakapokamilika kufanyiwa usanifu mwezi Aprili zitatafutwa fedha haraka ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami tukitambua kwamba ndio litakuwa lango kubwa la bidhaa zetu kwenda DRC. Ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; kwa kuwa barabara ya Iguguno kupitia Nduguti mpaka daraja la Sibiti inaunganisha Mkoa wa Singida na Simiyu na inapita makao makuu ya Wilaya.

Je, Serikali haioni haja ya kujenga kipande cha kilometa 42 kutoka Iguguno mpaka makao makuu ya Wilaya kwa mtindo wa build and design? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga barabara hii lakini daraja alilolisema tunajenga daraja la msingi na hili daraja ambalo amelisema, liko kwenye mpango wa kufanyiwa usanifu ili liweze kujengwa kwa kiwango cha zege.

Kwa hiyo, naomba baada ya hapa tukutane na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kuelekezana zaidi jinsi kazi hii itakavyofanyika. Ahsante. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante; tatizo lililopo Mpanda ni sawa sawa na tatizo lililopo kwenye Wilaya ya Kahama, Halmashauri ya Msalala Jimbo la Msalala; barabara inayotoka Bulyanhulu kwenda Kahama; barabara hii imekuwa ni mbovu sana mwaka jana imetengewa shilingi bilioni 3...

SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, swali langu ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii inayotoka Bulyanhulu kwenda Kahama kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Mbunge wa Msalala kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Bulyanhulu – Segesi – Kahama ni sehemu tu ya barabara inayoanzia Geita – Bukoli
– Bulyanhulu – Segesi - Kahama na kama alivyosema barabara hii imetengewa fedha, lakini niliwahi kujibu kwenye jibu la msingi swali lililopita kwamba kuna mazungumzo ambayo wenzetu wa Barrick wameonesha utayari wa kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami na mazungumzo bado yanaendelea. Kama watakwama basi Serikali itachukua hatua ya kuijenga barabara hiyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, ahsante; barabara ya kutoka Tabora – Mambari – Bukene – Itobo – Kahama ilishafanyiwa, usanifu wa kina na ilitengewa fedha kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami.

Je, ni sababu zipi zinafanya ujenzi huu usianze licha ya kuwa imeshatengewa fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Zedi Mbunge wa Bukene kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Tabora – Mambari – Ntobwa – Nzega imeshafanyiwa usanifu wa kina na ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha na itakapopatikana hiyo fedha, tutaanza kwa sababu tayari ipo kwenye mpango na ipo kwenye bajeti. Ahsante. (Makofi)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza; barabara ya Bunju B, Msitu wa Mabwepande mpaka Mbezi Mwisho ilipandishwa daraja kutoka TARURA kuingizwa TANROADS na Mheshimiwa Rais aliahidi kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Je, ni lini sasa Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Josephat Gwajima kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema barabara hii ilikuwa inahudumiwa na TARURA na kwa kuwa imepandishwa daraja naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge kuwa katika kipindi hiki cha bajeti tuweze kuhakikisha kwamba barabara hii imeingia kwenye mpango ili tunapoanza utekelezaji wa bajeti inayofuata barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kama Mheshimiwa Rais alipoipandisha na kuhakikisha kwamba inajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini barabara ya Airport kwenda Nyanguge yenye urefu wa kilometa 46 kupita Kayenze itawekewa lami kwa kuwa barabara hiyo ipo kwenye Ilani ya Uuchaguzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Matondo, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mwanza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Airport – Nyanguge ni kama by pass kwa upande wa magari yanayokwenda njia ya Musoma na ni kweli ipo kwenye mpango na Serikali inatafuta fedha. Tumewasiliana sana na Mheshimiwa Angelina Mabula ambaye ni Mbunge mwenyewe akiwa anaifuatilia hii barabara.

Mheshimiwa Spika, ninataka nimhakikishie kwamba bado ipo kwenye mpango na itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru pamoja na majibu ya Serikali naomba kuuliza swali dogo moja tu la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kazi kubwa sana iliyofanywa na Serikali ya kuboresha bandari ya Tanga na kwa sababu bandari ya Tanga kuwa na eneo dogo, ujenzi wa bandari kavu kwenye eneo la Korogwe ni jambo muhimu sana. Ni lini sasa Serikali itafanya hiyo tathmini ili kuwezesha bandari kavu kwenye eneo la Mji wa Korogwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Kwa sasa Serikali inaboresha na imewekeza sehemu kubwa sana kuboresha bandari ya Tanga ili kuweza kupokea mizigo na kusafirisha mizigo mingi. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi tulikuwa bado eneo la Korogwe halijabainishwa kuwa eneo la kujenga bandari kavu, na ndiyo maana Serikali imesema baada ya kupata hilo wazo la Mheshimiwa Mbunge ambaye kazi yake kubwa pia ni kuishauri Serikali tumelichukua na tutafanya tathmini ili tuone kama eneo hilo litafaa kujenga bandari kavu ambayo itakuwa na tija na endelevu, ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali, na ni matarajio ya wananchi wa Jimbo la Ukonga ya kwamba barabara hizi zitatekelezwa kwa wakati kama Serikali ilivyoagiza.

Mheshimiwa Spika, swali dogo la nyongeza; kwa kuwa Serikali inao mpango na barabara nyingi zimeahidiwa ikiwemo barabara ya Msongola – Mbande yenye jumla ya kilometa 4.95. Ni lini Serikali inatoa ahadi ya kuanza kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kwa niaba ya Mheshimiwa Jerry Silaa wa Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Msongola – Mbande hadi Mbagala (kilometa tano) sisi tunasema bado hazijajengwa kwa kiwango cha lami. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeanza mpango na tayari zabuni zimeshatangazwa. Tutaanza kuijenga kilometa mbili kwa mwaka huu wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. na mimi ninapenda kujua ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi – Shigamba ambayo ni kiungo cha mikoa ya Mbeya na Songwe kupitia Ileje, na pia ni kiungo kwenda Nchi jirani ya Zambia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbalizi – Shigamba tayari zabuni zinaandaliwa kuitangaza kwa ajili ya kufanya feasibility study na usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi kwa kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo mwaka huu tutahakikisha tunakamilisha feasibility study pamoja na usanifu wa kina, ahsante.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mwembe – Mbaga – Mamba ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Hayati Rais Dkt. Magufuli?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mwembe – Mbaga ambayo iko Same ni barabara ambayo iko kwenye miinuko. Tulichokifanya kwa sasa, kabla ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami ni kuainisha maeneo yote korofi na yenye miinuko ili tuweze kuyadhibiti na yaweze kupitika kwa mwaka wote, na baada ya hapo Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kufanya feasibility study na usanifu wa kina ili kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Murushaka kwenda mpaka Murongo, ahadi ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, kilometa 50, imeshatangazwa muda mrefu lakini mpaka sasa hivi haijaanza ujenzi; nini tatizo lake?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara haina shida, nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa tulishatangaza, mzabuni (mkandarasi) alishapatikana na tunategemea muda wowote ataoneshwa site ili aanze kutekeleza hiyo kazi, kilometa 50, kama zilivyoahidiwa na kama tunavyotegemea mkandarasi aanze kuifanya hiyo kazi. Ahsante.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Jiji la Dodoma ni jiji kama yalivyo majiji mengine na hivyo linapaswa kuwa na hadhi zote za jiji. Sasa swali langu; ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara za mitaani kwa kiwango cha lami kwa mitaa yote ya Jiji hili la Dodoma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lambert kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie kwamba jitihada kubwa sana zinafanyika kufanya kwamba barabara zote za Jiji la Dodoma zinafanyika. Tuna barabara za outer ring circuit na za inner ring circuit, lakini pia barabara zote ziko kwenye mpango kuhakikisha kwamba zinapanuliwa na kujengwa kwa kiwango cha lami ili kuhakikisha kwamba jiji linakuwa kweli na hadhi ya jiji, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Ni lini Serikali itaimarisha, kuboresha na kudhibiti korongo kwenye Mlima wa Mawono, barabara ya Unyoni kuelekea Maguu wakati tunasubiri utekelezaji wa ujenzi wa lami kama Serikali ilivyoahidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Benaya Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, korongo alilolisema naomba nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa Mkoa wa Ruvuma aende akalitathmini na aone kazi ilivyo ili tuweze kupata gharama na tuweze kulikarabati ili isije ikaleta madhara ya kukata mawasiliano ili tuweze kulikarabati kabla ya kuanza kujenga hiyo barabara ama kuifanyia usanifu kwa maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nina swali dogo la nyongeza kuhusiana na barabara inayotoka Mbagala kuelekea Temeke kutokea Kilungule - Mbagala kupitia Buza Kwa Mpalange; ni lini sasa itakamilisha ile lami? Kwa sababu wananchi wanapiga kelele sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara zetu nyingi za TANROADS na TARURA zinaingiliana. Lakini nitumie tu nafasi hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ni kuzijenga barabara zote kwa kiwango cha lami na kwa kuwa barabara zimeshaanza kujengwa, tunamhakikishia kwamba Serikali itazikamilisha hizo barabara, ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mlowo – Kamsamba kupitia Utambalila na Chitete ikiwa iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi mwaka 2025? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara Kamsamba – Utambalila – Chitete ni barabara ambayo ni sehemu ya barabara ya Mlowo – Utambalila – Kamsamba; barabara hizi ziko kwenye package moja. Kwa sababu tulishakamilisha usanifu, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya Buguni kuanzia Tengeru sokoni kupitia Kikwe hadi Mererani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni barabara ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa eneo hilo na Serikali ina mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Ikishakamilisha usanifu wa kina barabara hii tutaijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa wananchi wa Kondoa Mondo, walikuwa wanasubiria ujenzi wa barabara hiyo, sasa hivi inaonekana kwamba imekwepeshwa. Sasa Serikali ina mpango gani juu ya kuijenga barabara hiyo hiyo ambayo imeandikwa kwenye Ilani kutokea Mondo kwenda Kondoa - Bicha – Guseria kwenda kwa Mtoro?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, wananchi walikuwa na matumaini, kwamba kilomita hizi 400 zingepita kwenye Daraja la Mto Bubu, je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuharakisha ujenzi wa lile daraja ambalo litaunganisha barabara hii iliyokuwa inategemewa ili kuondoa kero na kuokoa maisha ya wananchi na mali zao vinavyopotea kila mwaka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Barabara ya kuanzia Goima – Mondo - Kondoa – Bicha, ipo kwenye Ilani na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri ya upatikanaji wa fedha barabara hii pia itajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ujenzi wa daraja katika Mto Bubu, Daraja la Mungui, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Kondoa kwamba tunajua changamoto ambayo ipo, upembuzi yakinifu wa daraja hili umeshakamilika na sasa hivi tutakamilisha usanifu wa kina. Meneja wa Mkoa ameshapewa kibali aandae pia na documents za kutangaza daraja hilo kuanza kujengwa. Kwa hiyo, litaanza kujengwa tu mara baada ya kukamilisha usanifu wa kina.
MHE. MWITA B. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ningependa kujua Barabara ya Bariri – Mgeta, ambayo ahadi yake ilitolewa na Mheshimiwa Rais, mwezi wa pili mwaka huu, ni lini itamaliza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bunda – Mgeta kama alivyoisema, iliahidiwa na viongozi na sisi kama Wizara pamoja na Serikali tunaendelea kutafuta fedha ili kutimiza hiyo ahadi ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina swali moja la nyongeza.

Swali hili ni kuhusiana na habari ya shilingi bilioni moja ambayo imetengwa. Unaweza kuona ni kiasi kidogo sana cha fedha, nilitaka nipate majibu na wananchi wa Jimbo la Kishapu wapate majibu kwamba kiasi hiki cha fedha tafsiri yake ni nini kwa sababu bilioni moja ni kiasi kidogo sana ili na matumini wawe wananchi wa Kishapu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Kishapu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kwa ukubwa wa barabara hii, hii fedha ambayo imetengwa haiwezi kuikamilisha, lakini nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge ni utaratibu kwamba barabara hizi hazijengwi kwa siku moja wala kwa mwaka mmoja na ndiyo maana mpango ambao tunautumia kwa kujenga barabara ni ku-raise certificate. Kwa hiyo, wakishaanza kila watakapokuwa wamefika hatua nyingine wanaandika certificate, wanalipwa na ndiyo utaratibu ambayo tumekuwa nao katika ujenzi wa barabara zetu baada kazi ana-raise certificate na Serikali inalipa hizo fedha. Kwa hiyo, ni barabara kuu tunalijua hilo na ndiyo maana tayari tumeanza kuandaa taratibu za kutangaza hiyo barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Mbuyu wa Mjerumani kupitia Magala hadi Mbulu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mbuyu wa Mjerumani kwenda Mbulu ni barabara ambayo ndiyo tumekamilisha usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi kwa kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge ipo kwenye mpango, tulichokuwa tunafanya ni kukamilisha usanifu na tukishakamilisha Serikali itaendelea kutafuta fedha ili kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Nakumbushia barabara ya kutoka Kibaoni – Mfinga inapita Mto Wisa inakuja kutokea Mloo, barabara hii ni muhimu sana kwa Mkoa wa Rukwa.

Je, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba nikubaliane na Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa kwamba barabara aliyoitaja inaunganisha Mkoa wa Mbeya na Rukwa hadi Katavi, ni barabara ambayo tayari upande mwingine imeshakamilika usanifu lakini bado tunaendelea kukamilisha usanifu wa kina kwa kipande kingine tayari tumeshaanza kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, ni lini Serikali itaendeleza ujenzi wa barabara ya lami iliyoishia katika Kijiji cha Elelai kuelekea Kamwanga inayounganisha Wilaya ya Longido na Wilaya ya Siha inayozunguka Mlima Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Magige, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ni barabara muhimu sana iko kule mpakani. Baadhi ya sehemu tumeshaikamilisha na sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kuiunganisha barabara yote kwa lami na iweze kupitika kwa urahisi. Ahsante.
MHE. IDDI KASSIM IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara inayotoka Solwa kuja Moktolio – Bulige - Ngaya mpaka Kahama ni barabara iliyoko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na inatakiwa ijengwe kwa muda mrefu sasa. Sasa swali langu ni lini fedha hizi zitatengwa ili barabara hii ianze ujenzi mara moja? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara niliyoitaja ipo kwenye mpango na ipo kwenye Ilani, kwa hiyo, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili ijenge kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi; nataka nijue ni lini ujenzi wa barabara wa Mbande - Kisewe - Msongola utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii itaanza kujengwa kama tulivyoipanga kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; barabara ya Bugene – Itela - Nkwenda mpaka Kaisho ambazo ni ahadi ya Mheshimiwa Hayati Rais Magufuli, kilometa 50. Ni lini barabara hii itaanza kujengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kutimiza hiyo ahadi.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, tumepata barabara ya mchepuo ya kilometa tatu ambapo mvua ikinyesha hali itakuwa mbaya zaidi. Je, Serikali ni lini itatujengea barabara ya lami kwa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fyandomo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mbeya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hiyo barabara tuliyojenga ni kwa ajili ya dharura ili kuepusha ajali zilizokuwa zinatokea. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango wa Serikali sasa ni kuijenga barabara hiyo ya lami. Kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha ili iijenge na liwe ni suluhisho la kudumu. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipatia fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa majibu ya Serikali yenye kutia moyo. Lakini tungependa kujua kutokana na wingi wa abiria katika Mkoa wa Kagera.

Je, ni lini shughuli ya kuwalipa fidia wakazi wa eneo lile kama mchakato wa kuanza ujenzi wa uwanja wa kimataifa wa Omukajunguti itafanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kutokana na wingi wa abiria unaokabili Uwanja wa Ndege wa Bukoba, je, Serikali haioni umuhimu wa kuanzisha miruko zaidi ya mmoja ili kukabiliana na mahitaji ya usafiri wa anga kwa wakazi wa Mkoa wa Kagera?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba kuna timu iliundwa na mwezi uliopita ilienda kutembelea eneo la Uwanja wa Omukajunguti ili kujiridhisha kama una uvamizi kiasi gani, ikiwa ni maandalizi ya kuanza kulipa fidia. Kwa hiyo taarifa itakavyotoka taraibu zitaanza ili wananchi waweze kulipwa na maandalizi ya ujenzi wa uwanja huu uanze.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la pili linalohusu miruko, suala la ndege ni biashara pia ni huduma. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Shirika la Air Tanzania wamesikia na watafanya tathmini kuona kama kuna umuhimu wa kuongeza safari zingine.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwa kunipatia nafasi.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa upanuzi wa uwanja wa Mkoa wa Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kibondo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wa Mkoa wa Kigoma kwamba nyaraka za zabuni kwa sasa ziko kwa Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya vetting ili kazi ya upanuzi wa uwanja huo zianze. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Ifakara ni mji unaokuwa kwa kasi sana na uwanja wake wa ndege ni dhoofu. Ni lini Serikali itakarabati Uwanja wa Ndege wa Ifakara ili ndege kubwa ziweze kutua?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asenga Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tulichukue. Hata hivyo niwaagize watu wa TAA na TANROADS wautembelee uwanja huo kwa ajili ya kuufanyia ukarabati. Ahsante.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa barabara ile inaunganisha na barabara ya Sengerema- Ngoma, je ni lini itafanyiwa usanifu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, barabara ya Sengerema- Kamanga imeshafanyiwa usanifu, leo ni miaka mitatu; je, ni lini itajengwa kwa lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tabasam Mbunge wa Sengerema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Sengerema- Ngoma haijafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na ipo kwenye Ilani. Tumemwagiza meneja wa Mkoa wa Mwanza aweze kuangalia kama kutapatikana fedha yoyote kwenye fedha ya maendeleo basi aielekeze kufanya usanifu wa barabara hii kwa sababu ni barabara fupi sana. Na barabara ya Sengerema – Kamanga Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Utegi-Shirati mpaka Kilongwe ni barabara ya kimkakati inayounganisha nchi mbili kati ya Tanzania pamoja na Kenya kwa kupitia Wilaya ya Rorya. Na kwa kuwa tayari upembuzi yakinifu wa barabara hii umeshakamilika nilitaka nijue ni lini sasa barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu kwa sababu inaunganisha Tanzania na Kenya. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua barabara yetu ya Ubena Zomozi-Ngerengere ya kilometa 10?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Taletale Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Mbena Zomozi imeshapata kibali kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami hizo kilomita alizozisema. Ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Swali la kwanza; kwa kuwa tunaelekea robo ya pili ya mwaka wa fedha sasa na jiografia ya Mlima Magara ni ngumu sana utekelezaji wake wakati wa mvua; je, Serikali imefikia hatua gani katika mchakato wa hiyo kilometa moja?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Barabara ya Magara – Mbulu ina jiografia ngumu kuliko sehemu yoyote nchini na hizo kilometa 44 zilizobaki zimefanyiwa usanifu tayari kwa miaka mitatu. Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza mpango wake wa lami wa kilometa 44 katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kuanzia Novemba mwaka huu barabara hii itakuwa imeanza kujengwa kwa kiwango cha zege kwa sababu taratibu zote za zabuni zimeshakamilika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuanza kujenga barabara yote, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kilichokuwa kimefanyika ulikuwa ni usanifu wa awali na atakubaliana nami kwamba wakati Makamu wa Rais anafungua Daraja la Magara mwezi Machi mwaka huu aliagiza barabara ile ikamilike na Juni mwaka huu ndiyo usanifu wa kina umekamilika. Kwa hiyo Serikali inaendelea kutafuta fedha ili ijenge kilometa hizi 44 kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa kumekuwa na ucheleweshwaji mkubwa wa utoaji wa tax exemption kwa wakandarasi, sasa ni lini Wizara ya Ujenzi watakaa chini na Wizara ya Fedha ili waweke mfumo mzuri utakaorahisisha wakandarasi hawa kupewa tax exemption mapema ili waweze kujenga barabara mapema ikiwemo Barabara ya Bulyanhulu mpaka Kahama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na maboresho mengi ya kuhakikisha kwamba malipo ya wakandarasi yanalipwa haraka na sasa hivi TRA hata mikoani wana uwezo wa kuchakata na kuharakisha malipo ya hawa wakandarasi. Hata hivyo, bado Serikali inaendelea kuboresha ili kuona namna bora zaidi ya kukamilisha malipo haya ya wakandarasi kwa muda. Ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nauliza Serikali, je, ni lini itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami wa Barabara ya Bigwa – Kisaki ya kilometa 78?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamisi Taletale, Mbunge wa Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bigwa – Kisaki (kilometa 78) ilishapata kibali na taratibu za kukamilisha zabuni hizo ilitangazwa, lakini itatangazwa tena kwa ajili ya kupata mkandarasi. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa kibali kilishatolewa, kwa hiyo ni taratibu tu za manunuzi ambazo zinaendelea ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali ina mpango gani wa kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya kutoka Nangurukuru mpaka Liwale inayopitia katika Majimbo ya Kilwa Kusini, Kilwa Kaskazini pamoja na Jimbo la Liwale?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Nangurukuru – Liwale ipo kwenye mpango kuijenga kwa kiwango cha lami na tayari usanifu ulishakamilika. Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo kwa kuwa usanifu umeshakamilika, Serikali ipewe nafasi na fedha ikipatikana barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Dongobesh – Dareda, ni lini itajengwa kwa kwiango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K.
MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii imeshapata kibali kuanza kujengwa kwa awamu kwa kiwango cha lami kuanzia Dareda kwa kilometa zisizopungua nane. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Tunaishukuru Serikali kwa kuendelea na ujenzi wa Barabara ya Ifakara – Kidatu na hasa tunaishukuru Wizara ya Ujenzi na TANROADS kwa usimamizi wa barabara hii. Je, Serikali ina mpango gani wa uwekaji wa taa za barabarani katika Barabara hii ya Ifakara – Kidatu kama Mheshimiwa Waziri Mkuu alivyoelekeza kwa zile barabara zinazopita katika vijiji?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asenga, Mbunge wa Kilombero, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru na kumpongeza kwa kutambua jitihada za Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inaendelea kujengwa sasa hivi kwa kasi tofauti na ilivyokuwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa sasa barabara zote zinazojengwa na hasa kwa kiwango cha lami, pale ambapo kuna miji mikubwa na midogo taa za barabarani zinatakiwa ziwekwe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu huo upo na itakapokamilika basi awamu itakayofuata itakuwa ni kuweka taa za barabarani. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza; ni lini Serikali itaanza upembuzi yakinifu wa Barabara kutoka Mfumbi – Matamba – Kitulo (kilometa 51) ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu ni ahadi ya Serikali na ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kama barabara ya uchumi ambako tunajua kunalimwa viazi vingi sana na mazao ya mbao. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ina mpango wa kuanza kuifanyia usanifu barabara hii ili kupata thamani ama gharama ya hiyo barabara na baadaye Serikali itafute fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Imekuwepo Barabara ya Makondeko – Kwembe – Kisokwa ambayo imekuwa ndani ya bajeti katika kipindi cha miaka miwili mfululizo, 2021/2022 na 2022/2023. Je, ni lini sasa Serikali itaanza kujenga barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mtemvu na atakubaliana nami kwamba tumefika kwenye jimbo lake. Barabara hii ni kati ya zile barabara ambazo zinapunguza msongamano katika Jiji la Dar es Salaam na ipo katika mpango wa kuanza kuijenga kwa awamu hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. SYLVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya TAMCO - Mapinga - Kibaha inayojengwa kiwango cha lami imekuwa inasuasua kwa muda mrefu, lakini pamoja na hilo wale wananchi waliopisha ujenzi wa barabara hii hawajalipwa fidia hadi leo kwa maana ya wananchi wa kata ya Tangini na Pangani. Je, ni lini wananchi hawa watalipwa fidia kama kwa mujibu wa sheria ulivyo?

Swali la pili barabara ya zamani kwa maana ya Dar es Salaam - Morogoro inayoanzia sasa Picha ya Ndege mpaka Mlandizi ni barabara ambayo ni kimbilio la wasafiri na wasafirishaji hasa barabara hii kubwa inapopata tatizo la ajali na kufunga barabara.

Sasa kwa umuhimu huo ni lini Serikali itaweka nguvu kurekebisha barabara hii ili iweze kupitika na kusaidia kutokuondoa msongamano wa barabara kubwa wakati kunapokuwa na ajali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Sylvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya TAMCO - Mapinga kumekuwa na ujenzi wa kusuasua na pia baadhi ya watu hawakulipwa fidia. Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalifahamu jambo hili na inalifanyia kazi kuhakikisha kwamba hawa watu wanalipwa na ujenzi huu unakamilika kwa muda kwa hii barabara ya TAMCO - Mapinga ambayo ni barabara muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu barabara aliyosema ambayo itakuwa ni msaada mkubwa sana kwa ajili ya kusaidia panapotokea changamoto kwenye eneo hili la picha ya ndege naomba nichukue suala la Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kwa maana ya Wizara kupitia TANROADS tutalifanyia kazi kuhakikisha kwamba barabara hii inaboreshwa iwe ni msaada pale ambapo barabara kuu inapopata changamoto inatusaidia kuhakikisha kwamba hatupati changamoto kubwa kwa maana ya kukwama. Ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Bujela -Masukulu na kuekelea Matebe na kutokea Kyela ni barabara muhimu sana kiuchumi kwa maana kokoa, chai inatoka maeneo hayo. Serikali haioni umuhimu wa kuijenga angalau kwa lami ili kuweza kusaidia uchumi wa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara zote tungependa tuzijenge kwa kiwango cha lami, lakini hatuwezi kuzijenga zote kwa wakati mmoja kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Kwa hiyo, tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali italichukua na ni mpango kwamba hizi barabara ikiwemo na hii barabara aliyoitaja kujengwa kwa kiwango cha lami, lakini kikubwa itategemea tu na uwezo wa bajeti ya Serikali. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali ina mpango wa kujenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Ndala kwenda Mwawaza kuliko na Hospitali ya Rufaa. Je, ni lini itaanza kutekeleza mpango huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge Viti Maalum Mkoa wa Shinyanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii itaanza kujengwa pale tu ambapo fedha itapatikana kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hiyo barabara muhimu. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru kwa kunipa nafasi.

Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kutoka Namanyere - Kilando mpaka Kipili kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Rukwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Namanyere hadi Kipili ambayo inaenda bandarini ni barabara muhimu na barabara hii iko kwenye usanifu, kwa hiyo baada ya kukamilisha usanifu wa kina Serikali itatafuta fedha ili ianze kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi naomba kuuliza barabara ya kutoka Masumbwe kwenda Geita Makao Makuu ya mkoa ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Maganga, Mbunge wa Mbogwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masumbwe kwenda Geita imeshafanyiwa usanifu wa kina na sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Spika, ahsante naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri ni lini barabara ya Bonyokwa - Kimara itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah, Mbunge wa Segerea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba amefika mara kadhaa Wizarani na Mheshimiwa Waziri pamoja na TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam wamemuahidi na mimi nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo kutoka Bonyokwa kwenda Kimara ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, mimi nishukuru tu kwamba majibu ni mazuri, lakini siyo majibu ya swali la msingi.

Swali la msingi linauliza ni lini barabara hii inaanza kujengwa?

Kwa hiyo swali langu mimi la kwanza la nyongeza ni lini barabara hii inaanza kujengwa? Na swali la pili ni lini barabara hii inaanza kujengwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante na napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mbunge wa Maswa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la msingi ni lini Serikali itajenga barabara kutoka Sibiti hadi Salama, Sayaka, Kisamba nimejibu kwamba ili uanze kuijenga barabara lazima ifanyiwe upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, na katika hiyo barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge kuna eneo ambalo tumesema kilometa 71 ipo kwenye mpango wa EPC na tayari taratibu zimeshaanza.

Kwa hiyo, ni kwa maandalizi ya kuijenga na vipande ambavyo vimebaki kutoka Mwandoya Junction ambapo ni Goboko kwenda Kisesa hadi Itilima mkandarasi ameshapatikana kwa ajili ya kuanza kuifanyia usanifu, hayo yote ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami na baada ya kuikamilisha ndipo sasa barabara hiyo tutajua gharama za ujenzi na tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nami naomba niulize swali la nyongeza.

Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami inayotokea Duto kuelekea Nyashimo kupitia Shigala, Malili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Duto - Nyashimo itajengwa tu pale ambapo fedha na bajeti itaruhusu kwa sababu tayari ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ni lini barabara ya Mnivata kwenda Masasi itajengwa ni kwa nini haijengwi wakati pesa bado ipo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wote ambao barabara hii inapita Mnivata - Newala hadi Masasi yenye urefu wa kilometa 160 kwamba tayari taratibu zote zimeshakamilika kwa maana ya maandalizi ya zabuni na barabara itakuwa na loti mbili na katika ujenzi huu pia Daraja la Mwiti limeunganishwa na tayari tunachosubiri ni wenzetu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika watupe no objection kwa sababu ndiyo wanaoijenga hii barabara. Kwa hiyo, muda si mrefu barabara hii itatangazwa kwa ajili ya kuijenga yote kilometa 160. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi amekuwa akiniahidi sana kila mara kwamba pesa ya upembuzi yakinifu itakapopatikana barabara ya kutoka Kahama - Nyang’hwale itawekwa ndani ya mpango.

Je, ni lini pesa hiyo itapatikana na kuwekwa ndani ya mpango hiyo barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein Nassor Mbunge wa Nyang’hwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa tuweze kuangalia kitabu cha bajeti ili tuone. Naamini kwamba hii barabara itakuwa imetengewa fedha kwa ajili ya mpango kwa mwaka huu. Na kama kutakuwa haijatengwa basi tuangalie Wizara nini cha kufanya ili kuiwekea kwenye mpango wa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara hii. (Makofi)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwakuwa Serikali imetangaza zabuni ya ujenzi wa barabara ya Morogoro, Njombe boda walau kwa kilometa 100 route one na route two. Je ni lini kazi hii itaanza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Mlimba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye hatua za manunuzi. Najua Mheshimiwa Mbunge anaifuatilia; ipo kwenye hatua za manunuzi kwa ajili ya kuanza kuijenga hiyo barabara kwa hivyo ipo kwenye hatua mbalimbali za manunuzi ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, barabara ya Kolandoto Munze Mwingunge yenye kilometa 63 imekuwepo kwenye mpango wa utekelezaji kwa maana ya ujenzi katika kiwango cha lami kwa mwaka 2021/2022. Mwaka 2021/2022 haikuweza kutekelezwa. Je, nini mpango wa Serikali kwa mwaka 2022/2023 kuhakikisha kwamba unatekelezwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Butondo Mbunge wa Kishapu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kolandoto hadi Lalago kama alivyotaja hizo kilometa 62 imepewa Bajeti kwa ajili ya kuanza kujenga kwa kiwango hiki; kwa hiyo tusubiri tutakapoanza utekelezaji wa bajeti. Ahsante.
MHE. MWANTATU MBARAK KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake. Hata hivyo, pamoja na majibu hayo mazuri pia napenda kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.

(i) Je, ni maeneo gani mahsusi ambayo Serikali imeyazingatia katika utumiaji watu wenye ulemavu katika mabasi hayo?

(ii) Kwa kuwa mmesema mmezingatia; je, ni kwa nini hakuna utaratibu maalum ambao umezingatia watu wenye ulemavu wakati wanapofika vituoni na wanapotaka kutumia usafiri huo kwa kupanda mabasi hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza tukiri kwamba hapo awali miundombinu mingi ambayo ilikuwa ikijengwa ilikuwa haizingatii sana mahitaji ya watu wenye ulemavu ikiwa ni pamoja na kwenye hospitali, shule na majengo mengi. Hata hivyo, sasa imekuwa ni utaratibu wa Serikali kwamba miundombinu yote inayojengwa, iwe majengo iwe wapi lazima izingatie watu wote wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, kwenye masuala la usafiri; na tumetoa mfano wa mwendokasi; Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba hata ujenzi wa barabara na hasa kwenye vituo mtu yeyote mwenye mahitaji maalum, na hasa watu wenye ulemavu, yale mabasi yamejengwa na yametengenezwa kiasi kwamba yapo kwenye usawa. Kwamba anatoka anaingia, na hata kama ana Wheelchairs ana uwezo wa kuingia kwenye mabasi hayo katika vituo vyote. Lakini pia kwenye mabasi kumekuwa na nafasi na kumekuwa na viti maalum vya watu wenye mahitaji hayo; kwa maana ya watu wenye ulemavu wazee na hata wajawazito; na hata rangi ya viti imekuwa ni tofauti. Pia kumekuwa na utaratibu wa watu kuingia kwa foleni

Mheshimiwa Spika, pengine nitumie nafasi hii kusema kwamba, kunapokuwa na watu wenye ulemavu wanaposafiri wanatakiwa wawe na mstari wao na wawe wa kwanza kuingia, na viti vyao visikaliwe na watu wengine. Sasa, suala hili tunataka pia liende kwenye mabasi mengine ya umma, kwa mfano daladala na hata yanayokwenda mikoani. Ahsante. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Kwakuwa Serikali sasa inaandaa kanuni za ujenzi, kwa maana ya Billing regulation, nini commitment ya Serikali kuhakikisha majengo yote yanayojengwa kwenye nchi yetu yanazingatia mahitaji wa watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kama nilivyosema kwenye maelezo yangu ya awali, kwa sasa majengo na ujenzi wowote unajengwa wa Serikali lazima uzingatie watu wenye mahitaji maalum. Na kwa suala la hizo regulation nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba lipo na linaendelea kufanyiwa kazi. Lakini hadi sasa hivi hakuna ujenzi wowote unaojengwa bila kuzingatia hayo mahitaji maalum. Ahsante (Makofi)
MHE. ABDULLAH ALI MWINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majawabu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa Uber inachangia kwa kiasi kikubwa sana ajira nyingi za vijana; je, Serikali haioni kwamba ajira ya vijana ina mchango chanya zaidi kushinda hizi tozo ndogo ambazo Serikali imeziweka?

Swali la pili; kwa kuwa Uber ni kampuni ya teknolojia na siyo kampuni ya usafiri, Uber ulimwengu mzima haina gari hata moja, inawezesha watu wenye magari kuweza kufanya biashara ya usafiri wa taxi kirahisi na kwa kuhuda nafuu.

Je, taasisi ya LATRA (Mdhibiti wa Magari ya Ardhini) ni taasisi sahihi kufanya majadiliano na kampuni ya Uber? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu mawali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Abdullah Ali Mwinyi, Mbunge wa Mahonda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba Uber pamoja na mashirika mengine ambayo yalikuwa yanatoa huduma za taxi mtandao yanatoa ajira kubwa kwa vijana, lakini pia yanatoa huduma kwa wasafiri. Kilichopelekea kusitisha huduma kwa kampuni hii ya Uber na Bolt ilikuwa ni baada ya LATRA kuona uwezekano wa wao kupunguza kamisheni ambapo walikuwa wanatoa zaidi ya asilimia 25 na kukawa kuna malalamiko ya wamiliki wa taxi ambapo waliona kamisheni ile sasa hawafanyi kazi vizuri ndiyo maana wakasimama.

Kwa hiyo ilikuwa ni kuona ni namna gani wamiliki wa taxi watapata faida lakini wamiliki wa haya makampuni ya taxi mtandao watapata faida, lakini pia bila kumuumiza abiria.

Mheshimiwa Spika, tarehe 5 mpaka 8 Septemba, 2022 LATRA, wamiliki wa hizi taxi pamoja na wasafirishaji wengine wamekaa na wamekubaliana kupata muafaka na kabla ya mwisho wa mwezi huu Serikali itatoa taarifa maana kumekuwa na mazungumzo mazuri ili kuwa na win win situation kwa msafiri, mwenye taxi lakini na kampuni hizi ambazo zinasimamia huu usafiri wa taxi mtandao, ahsante.
MHE. EDWARD K. OLELEKAITA: Mheshimiwa Spika, sana, na niseme wazi kabisa kwamba nashukuru sana majibu ya Serikali ni mazuri sana sana. Pamoja na hayo Mheshimiwa Waziri natarajia kwamba hiyo barabara mtaanza kujenga kutoka Kongwa, Kwenda Kiteto mpaka Arusha. Swali la nyongeza, ni lini hasa kwa mipango yenu, baada ya hii process ya kufungua tenda, ninyi mmepanga lini sasa ujenzi huu uanze, ni Novemba, Desemba, Januari? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Edward Olelekaita, Mbunge wa Kiteto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niishukuru Serikali kwa kuipongeza Serikali kwa hatua ambazo inaendelea kuzichukua. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya Serikali ni kwamba taratibu zimeshaanza, na kama makampuni haya mojawapo litakidhi vigezo, litapewa hiyo zabuni, kwa hiyo taratibu za manunuzi zitaanza ili kuanza ujenzi huo kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kwa kuwa barabara ya Mlowo Kamsamba, ina umuhimu mkubwa sana wa kiuchumi kwa wananchi wa Wilaya ya Mbozi pamoja na Momba. Naomba kufahamu sasa, ni lini ujenzi wa kiwango cha lami utaanza katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Songwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mlowo Kamsamba, imeshafanyiwa usanifu wa kina na Serikali inatafuta fedha ili barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Sale kuelekea Mto wa Mbu kwa kiwango cha lami, ukizingatia barabara hii ni muhimu kwa shughuli za utalii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Valentine Magige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Mto wa Mbu – Loliondo hadi Sale ni barabara ambayo tumeanza kujenga kipande cha Waswaswale na kipande kilichobaki tayari usanifu umekamilika na Serikali sasa inatafuta fedha ili kuijenga barabara hiyo yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza; barabara ya Makofia – Mlandizi – Manarumango mpaka Vikumburu, ni lini itaweza kujengwa kwa kiango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Makofia – Mlandizi – Mzenga hadi Vikumburu ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango wa lami.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuuliza, Serikali imefikia wapi maandalizi ya ujenzi wa barabara kutoka Lumecha – Kitanda – Malinyi – Kilosa - Kwa Mpepo hadi Ifakara kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ambayo inaanzia Lumecha – Malinyi kuja Ifakara, ipo kwenye Mpango kama nilivyojibu kwenye swali la msingi; na jibu lake ni hilo hilo kwamba tayari wazabuni wameshaoneshwa, hiyo barabara, nayo imewekwa kwenye mpango wa EPC+F. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu ya Serikali yanayotia faraja. Nina swali moja la nyongeza. Naomba kufahamu na kauli ya Serikali kuhusiana na kukamilika kwa ujenzi wa barabara hii ifikapo mwaka 2025.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge wa Viti Maalum, Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tunayoitekeleza sasa hivi na imeeleza wazi kwamba lazima tuifanyie usanifu wa kina. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Makanika ambaye amekuwa akiifuatilia sana hii barabara kwamba tutahakikisha tunaifungua yote na baada ya hapo tutaanza kuifanyia usanifu wa kina baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu wa barabara hii.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Kipande cha barabara kinachotoka Uvinza kuelekea Malagarasi ujenzi wake unasuasua sana kwa muda mrefu. Napenda kujua nini tatizo la Serikali kufanya kipande hicho cha barabara kisikamilike?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilikuwa inasuasua, lakini sasa nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ya Uvinza hadi Malagarasi yenye urefu wa kilometa 51, kasi imeongezeka baada ya kuondoa changamoto zilizokuwepo. Ni matumaini yetu kwamba Mkandarasi huyu ataikamilisha barabara hii ndani ya wakati. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itafanya upanuzi wa barabara ya Moshi – Arusha kuanzia Tengeru – USA – Moshi Mjini – Himo mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii imetengewa fedha kuijenga, kwa maana ya kuikarabati, ikiwa ni pamoja ya kujenga daraja la Mto Karanga. Kwa hiyo, taratibu zinaendelea ili kuanza kuijenga hii barabara ikiwa ni kuikarabati sasa kwa kiwango kikubwa kwa mwaka huu wa fedha. Ahsante.
MHE. AHMED A. SALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa barabara hii ni muhimu sana, inaunganisha wilaya tatu, kwa maana ya Kahama, Shinyanga pamoja na Misungwi, na kwa kuwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ni mazuri lakini kwa namna ambavyo wameanza, ni jambo jema sana na namshukuru sana kwa sababu hatua za awali zinaonesha kwamba barabara hii tayari imeanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kama Serikali itaendelea kujenga kilometa 5.6, maana yake tutachukua zaidi ya miaka 20 kwenye ukamilishaji wake. Swali la kwanza; je, mwaka huu wa fedha kwanini Mheshimiwa Naibu Waziri, au Wizara hii isiongeze fedha angalau kilometa zaidi ya 20 au 30 ili barabara hii iweze kuonyesha mwelekeo wa kukamilika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa barabara hii, ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi wa 2015-2020 na 2020-2025, ilani ya chaguzi mbili na kwa kuwa barabara hii ni muhimu sana. Je, kwanini Serikali isiweke na kuonesha commitment kabisa ya moja kwa moja, ikatenga fedha kwenye ukamilishaji wa barabara hii, ikajengwa mpaka kukamilika kwake kabisa kabla ya mwaka 2025?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ahmed Ally Salim, Mbunge wa Solwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Solwa, kwa jinsi anavyofuatilia ujenzi wa barabara hii; na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunachokifanya ni kile ambacho tumekipata na fedha inayopatikana kwa kiasi chochote sisi tutaendelea kujenga, tunapunguza.

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuijenga barabara hii mihimu ambayo ni njia ya mkato kutoka Mwanza kwenda Kahama. Kama alivyoainisha, imeainishwa kwenye Ilani ya Uchaguzi. Tunaamini ndani ya mwaka huu, katika miaka inayokuja, barabara hii itatengewa fedha ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kadri fedha itakavyopatikana. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Swalli langu dogo la nyongeza, barabara ya Makete-Mbeya-Isionji, ni barabara ambayo tayari upembuzi yakinifu, hatua za manunuzi, na hata upekuzi wa kampuni iliyoshinda umeshafanyika. Mheshimiwa Waziri mbele ya Mheshimiwa Rais alituahidi mwezi wa tisa mkandarasi atafika site.

Je, ni lini mkandarasi atasaini mkataba ili aanze kujenga barabara hii ambayo ni uti wa mgongo wa uchumi wa Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara anayoitaja Mheshimiwa Festo ilitangazwa, lakini ilikosa Mkandarasi kwa sababu ya udogo, Mheshimiwa Rais akaongeza kilomita. Barabara hii ilishatangazwa na tayari mikataba imeshaandaliwa. Tunapoongea sasa hivi iko kwa Mwanasheria Mkuu kwa ajili ya kuifanyia vetting na tunategemea mara itakapotoka mwezi huu, basi mikataba hiyo itasainiwa ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza naishukuru Serikali kwa barabara hii ya kuanzia Magole hadi Tuliani.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu jibu hili limekuwa la muda mrefu tangu 2010 mpaka sasa hivi mnaendelea hivyo hivyo, ndiyo jibu hilo hilo na kipande ni kilomita102 tu.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutenga bajeti kwenye kipande hiki cha Km 102 kwenye bajeti ijayo?

Swali langu la pili; je, barabara ya Lupilo mpaka Mahenge ni lini nayo itajengwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshaanza kuijenga hii barabara hizo kilomita na hata katika bajeti ya mwaka kuna fedha imetengwa kwa ajili ya barabara hiyo, lakini Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa iko kwenye mpango tunaweka katika miaka inayokuja ya bajeti tutaendelea kutenga fedha ili kuikamilisha barabara yote hii.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili kwa barabara ya Lupilo – Mahenge, barabara hii ni kati barabara kuu kwa maana ya trunk road na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wako Wakandarasi ambao tayari wameshapita Lupilo – Mahenge kwa ajili ya kuangalia kama itajengwa kwa mpango wa EPC. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii pia Serikali inategemea kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Iringa kwenda Ruaha National Park, tayari ilishapewa fedha kwa maana zile fedha za mkopo.

Je, ni lini sasa Serikali itatangaza tender ili hiyo barabara ianze kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya kwenda Ruaha National Park Lusembe ina Kilomita 104 na inafadhiliwa na World Bank. Ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zote za kuandaa zabuni zimeshakamilika na muda wowote itatangazwa kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami barabara yote. Ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Mkuyuni kupita Maina mpaka Mwatex yenye Km 11 tayari usanifu wake umekamilika.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hiyo kwa lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K.
MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Furaha, Mbunge wa Viti Maalum – Mwanza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ya Mkuyuni hadi Maina imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, Wizara ya Ujenzi kwa kusaidiana na TAMISEMI tunatafuta fedha ili kuijenga barabara hii muhimu ambayo pia itakuwa kama bypass ya kuingia Mjini Mwanza. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zinaendelea, kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Njiapanda - Rugali – Ndembe – Longa Km. 10, kwa mbele kuna lami lakini kipande hiki hakina lami. Je, ni lini Serikali itaunganisha kipande hiki kutoka Mbinga Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Benaya Kapinga, Mbunge wa Mbinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoisema ni kweli ilijengwa mbele kwa sababu ya changamoto ya huko ilikojengwa ili kuhakikisha kwamba inapitika. Sasa hivi nimuhahakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili kukamilisha hiko kipande kilichobaki kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nilitaka kuuliza, kwa kuwa mchakato wa ujenzi wa barabara inayotoka Kakola kwenda Kahama umekalimika. Sasa ni lini na nini kimekwamisha Wizara kutangaza barabara hiyo ili ianze ujenzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge tumekutana naye sisi na Wizara lakini pia na watendaji wa TANROADS. Ni barabara ambayo kweli fedha imeshapatikana, taratibu zinaandaliwa ili kuitangaza barabara hiyo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo mwaka huu wa fedha itaanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami barabara kutoka Babati-Galapo-Kimtoro hadi Kibaya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum Manyara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Babati- Galapo kwenda Kibaya, tuanakamilisha usanifu wa kina; na mwaka huu itakamilika na baada ya hapo Serikali itaanza kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa sasa usanifu wa kina unaendelea kukamilishwa. Ahsante.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya kutoka Mnivata-Tandahimba-Newala-Masasi kilometa 160 tunafahamu kwamba fedha zake zimepatikana na kipindi cha mvua karibia kinaanza.

Je, ni lini sasa ujenzi utaanza rasmi wa barabara hii kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Mtanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii inafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika, taratibu zote za zabuni na kuandaa zimeshakamilika. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zote za manunuzi zitakavyokuwa zimekamilka, barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni kwenye ziara ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Kigoma, Wizara ya Ujenzi imetoa taarifa kwamba mna mpango wa kuupanua uwanja huo running way yake kutoka 1.8 kilometa na kuja kilometa 3.1; na wananchi wamepata taarifa hizo, lakini mpaka sasa hawajui ni eneo gani mtalichukua la wananchi.

Je, ni lini Wizara yako itakwenda ku-earmark maeneo ambayo yatayachukua, ili maeneo ambayo hamyachukui wananchi waendelee na shughuli zao za maendeleo?

Je, baada ya kuyachukuwa, mtaweza kulipa fidia kwa wakati tofauti na ilivyokuwa hapo nyuma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kilumbe Shabani Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli ahadi imeshatolewa, lakini pia nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari hata usanifu Wizara imeshafanya tayari, kutoka kilometa 1.8 mpaka kilometa 3.1. Kuhusu fidia, tayari taratibu zinaendelea ili mara taratibu, na hasa tunataka uwanja utakapoanzwa kujengwa kwa awamu ya kwanza kwa uwekezaji wa fedha ndipo awamu ya pili itakapoanza kupanua uwanja.

Kwa hiyo nikuhakaikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuanahitaji sana huo uwanja kuwa mrefu ili kupokea ndege. Serikali imejipanga kulipa fidia kwa wakati na kuanza kujenga, na taratibu zitakapoanza tutakuja kuwajulisha wananchi, wapi uwanja huo utapita. Ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa Serikali iliweka mpango wa kujenga viwanja katika mikoa kumi na moja, ukiwemo Mkoa wa Singida. Sasa nataka kujua ni lini ujenzi huu wa Uwanja wa Ndege Mkoa wa Singida utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli mpango upo wa kujenga Uwanja wa Singida na kwa sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza kufanya feasibility study ya Uwanja wa Singida. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’TA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali.

Je, ni lini uwanja wa ndege wa Sumbawanga Mjini utaanza kujengwa? Nataka commitement ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ta, Mbunge wa Rukwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi nililotoa, jibu hili linafanana kabisa na swali la Mheshimiwa Bupe. Tuna viwanja vinne ambavyo ni Kigoma, Sumbawanga, Tabora na Shinyanga, ambavyo vyote vinafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Ulaya. Pia, huyu mfadhili ameshatoa fedha na muda wowote uwanja huu, kama nilivosema wa Kigoma, nao utaanza kujengwa ikiwa ni pamoja na Uwanja wa Tabora na Shinyanga. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Uwanja wetu wa Iringa ni uwanja ambao tayari umeshawekwa jiwe la msingi na Mheshimiwa Rais;

Je, ni lini sasa utakamilika kwa sababu ujenzi umechukuwa muda mrefu sana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uwanja huu unaendelea kujengwa lakini pia uwanja huu World Bank imekubali kuufadhili, na kwa kuwa unaendelea. Kama kulikuwa na changamoto za kuchelewa, nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kasi imeongezeka na tuna hakika uwanja utakamlishwa kwa sababu mkandarasi yupo site na anaendelea na kazi. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Mkoa wa Simiyu upo kwenye ilani na eneo tayari limeshatengwa,

Je ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Uwanja wa Ndege Mkoa wa Simiyu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Simiyu, kama, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Uwanja wa Simiyu unatakiwa Kujengwa na mwaka huu tumetenga fedha kwa ajili ya kufanyia usanifu. Ahsante
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Lindi sasa hivi kuna gesi ambayo tunategemea itakuwa inawekezwa pale.

Je ni lini Uwanja wa Ndege wa Lindi Mjini utatatengenezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pathan, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Lindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Uwanja wa Lindi upo kwenye mpango, na katika bajeti hii upo kwenye mpango wa kuanza taratibu za kuujenga. Ahsante.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali. Nataka niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru sana Serikali kutuletea barabara ya lami, lakini ilishafanyika tathmini lakini wananchi wanasubiri malipo. Kwa sababu mchakato unaendelea, je tathmini italipwa lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu barabara hii inahusisha Majimbo mawili, Jimbo la Sengerema na Jimbo la Buchosa, je Serikali iko tayari kuchukua ushauri wa wananchi wa Buchosa, kwamba ujenzi wa barabara hii uanzie Buchosa kuelekea
Sengerema badala ya Sengerema kuelekea Buchosa?
(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eric Shigongo, Mbunge wa Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilimuelewa kuhusu tathmini, nadhani ni fidia, italipwa lini? Kama nilimuelewa ni kwamba fedha ambazo tumetenga, kitu cha kwanza itakuwa ni kulipa fidia ya wananchi ambao watapisha ujenzi huo, halafu barabara itaanza kujengwa. Kwa hiyo, itakuwa ni hatua ya kwanza ya kufanywa kabla ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu ushauri alioutoa, kwa mujibu wa barabara ilivyo ni Sengerema-Nyamazugo- Nyehunge; hili suala ambalo tayari hata zabuni kama zimeshatangazwa, maana yake zinataja kuanzia wapi kwenda wapi. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, pamoja na kwamba majimbo ni hayo mawili lakini barabara itaanzia huku tulikoitaja na kwenda pale inapokwisha kwa sasa. Ahsante sana.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Ninapenda kutaka kujua jibu la uhakika leo, ni lini barabara ya kutoka Kolandoto-Kishapu-Lalagwa hadi Meatu itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum Simiyu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumetenga fedha kuanza ujenzi wa Kolandoto hadi Lalago, bababara hii ambayo ni barabara kuu na tutaanza kwa kilometa 10 kwa sababu fedha tumetenga katika bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. ATHUMANI A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniruhusu na mimi niulize swali la nyongeza. Barabara ya Tabora - Mambali ambayo ufanisi wake umekwishafanyika siku nyingi, lini itaanzwa kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Tabora - Mambali tulishakamilisha usanifu wa kina na fedha tumetenga; na Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga hii barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Ipo ahadi ya kujenga kwa kilometa kumi kumi barabara kutoka Lushoto mpaka Mlalo. Je ni lini ahadi hiyo itaanza kutekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli ahadi ilishatolewa na Serikali inatafuta fedha ili kuanza ujenzi wa hiyo barabara kwa kilometa kumi kwa kiwango cha lami. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami, tumeshaanza, tumeshafika Magamba tukiwa tunaelekea Mlalo. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Barabara ya Zamahero-Babayo- Makorongo hadi Donsee ndicho kipande pekee yake kitakuwa sasa hakina lami, ukizingatia barabara ya Kibarashi - Handeni hadi Singida inajengwa na ni kibarabara cha kilometa 18 tu, nataka kujua Serikali mna mpango gani wa kutumalizia hiko kibarabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, alichosema ni kweli, barabara hii tutaijenga kwa kiwango cha lami lakini itategemea na upatikanaji wa bajeti. Kwa hiyo, Serikali inalifahamu na inaendelea kutafuta fedha ili kukamilisha hicho kipande ambacho ndicho kilichobaki. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ambayo ipo kwenye ilani na ipo kwenye mpango wa maendeleo, kutoka Mtwara - Pachani - Rusewa na Rasi-Tunduru barabara hiyo ambayo ni barabara ya ulinzi, na Naibu Waziri uliitembelea na kuona umuhimu wa barabara hiyo ambayo ina viijiji visivyopungua 40?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli alichosema, barabara hii tumeitembelea na ni barabara muhimu ina kilometa zisizopiungua 300. Tumeshakamilisha usanifu wa kina na kabla ya kuanza tumeainisha maeneo yote korofi kwanza na madaraja ili tuweze kuyajenga wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote hii muhimu kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa majibu yanaendelea kutolewa haya haya kila tukiuliza swali; je, nini kauli ya Serikali kuhusu lini uwanja huu utaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imeshakwenda hatua kubwa mbele, tayari tumeshathamini na tayari maandalizi ya malipo ya watakaopisha mradi huu yako yanafanyiwa kazi na tumeahidi kama Serikali kwamba baada ya kukamilisha suala hilo, ujenzi wa Uwanja wa Simiyu utaanza. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri swali nyongeza kwamba kwa kuwa barabara hii ilitajwa kwenye Ilani ya Uchaguzi wa mwaka 2015/2020 haikutekelezwa; ikatajwa kwenye Ilani ya Uchaguzi ya 2020/2025 na mpaka sasa hivi tunavyozungumza bado hakuna mchakato wowote wa barabara hii.

Nini kauli ya Serikali kwa wananchi wa Jimbo la Singida Magharibi na wananchi wa Mkoa wa Singida na Iramba kwa ujumla juu ya barabara hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali na kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi na kama alivyosema imetamkwa kwenye Ilani, Serikali inasema inategemea kutangaza zabuni kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami mwishoni mwa mwezi huu wa kumi na mbili kwa ajili ya kuanza kuijenga yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makambako - Songea tunajua kipande cha Songea mpaka mpaka na Njombe tayari kimeishapata mpango wake. Lakini kutoka mpakani mwa Songea na Njombe mpaka Makambako Serikali ina mkakati gani kuhusiana na kipande hiki cha barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kufanya matengenezo makubwa kwa barabara yote ya Makambako - Njombe hadi Songea. Kwa sasa kama alivyosema mpakani mwa Njombe na Ruvuma tayari tumeishapata fedha na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kufanya matengenezo makubwa kwa kipande ambacho kimeharibika sana kati ya Makambako - Njombe hadi mpakani mwa Mkoa wa Ruvuma, ahsante. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi.

Je, Serikali ina mpango gani wa barabara ya kuunganisha Mkoa wa Singida na Mkoa wa Simiyu kupitia Daraja la Sibiti?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Singida na Mkoa wa Simiyu kupitia Daraja la Sibiti hivi ninavyoongea barabara zote tatu ziko kwenye kukamilisha usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami kuanzia Ulemo kwenda Sibiti, lakini pia kuanzia Iguguno kwenda Sibiti wakandarasi wako tayari wanafanya usanifu kwa ajili ya maandalizi ya kujenga kwa kiwango cha lami kuunganisha hiyo mikoa miwili, ahsante.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Je ni lini barabara ya Karatu - Njia Panda kwenda Mang’ola - Matala hadi Lalago ambayo pia ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020 itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyotaja kutoka Karatu - Mang’ola hadi Sibiti ni barabara kuu. Hata hivyo tumeisha kamilisha usanifu na Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga hiyo barabara ambayo inapita sehemu muhimu sana ya uchumi na hasa kilimo cha vitunguu, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kuiuliza Serikali; je, ni lini barabara yetu ya Bigwa - Kisaki ya kilometa 78 itaanza matengenezo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Taletale, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilitangazwa, lakini kilometa zilikuwa chache na sasa barabara hii tunategemea kuitangaza muda wowote kuijenga kwa kiwango cha lami na tuko kwenye hatua za mwisho za manunuzi na barabara hii nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge itatangazwa mwaka huu wa fedha na itaanza kujengwa hizo kilometa 78, ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona; barabara ya kutoka Kibena kwenda Madeke barabara hii ipo kwenye Ilani na Mheshimiwa Rais, juzi alisema barabara hii itajengwa kwa lami na Mbunge wa Lupembe amekuwa akizungumza mara kwa mara. Nini kauli ya Serikali juu ya barabara ya Kibena - Madeke? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna maelekezo ambayo tumeyapata kwamba barabara hii ya Kibena junction - Madeke hadi Mlimba, Ifakara ijengwe kwa kiwango cha lami. Upande wa Morogoro ambako inakwenda tayari tumeshatangaza zabuni na upande wa Kibena kwenda Madeke ipo kwenye usanifu chini ya African Development Bank, lakini pia tunategemea tuanze kuijenga kwa kilometa chache kuanzia mwaka huu wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya swali hili ambayo yanaonekana yanatia moyo kwamba kuna majadiliano. Lakini niiombe Serikali majadiliano hayo yasichukue muda mrefu sana. Pamoja na majibu haya mazuri na swali moja la nyongeza.

Katika kuchochea uchumi shirikishi na shindani kuna barabara ndani ya Jimbo la Busanda kutoka Katoro kupita Kaseme kwenda Ushirombo, Jimboni Bukombe; je ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo ambayo imeishafanyiwa upembuzi yakinifu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Tumaini Magessa, Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Katoro hadi Ushirombo imeishafanyiwa usanifu na sehemu ya barabara hii inatekelezwa na Mpango ama Mradi wa RAIS, lakini sehemu iliyobaki itaendelea kuhudumiwa na TANROADS na Serikali ina mpango wa kutafuta fedha kukamilisha barabara yote kipande kitakachobaki baada ya kile kipande kitakachojengwa na Mpango wa RAIS kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Mkomazi – Mnazi - Umba junction Maramba hadi Tanga iko katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ukrasa wa 177 kwamba ijengwe kwa kiwango cha lami; je, ni lini sasa mchakato wa kuanza upembuzi yakinifu utaanza katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shangazi, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja inayounganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Kilimanjaro iko kwenye Ilani na utekelezaji wa Ilani unaendelea. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tunahakika kwamba tutaanza usanifu wa kina baada ya kufanya upembuzi katika kipindi hiki cha miaka mitano katika utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nakushuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliahidi kuwajengea Wananchi wa Jimbo la Nkenge Wilaya ya Misenyi barabara ya Mtukura kwenda Minziro na nikupongeze Mheshimiwa Naibu Waziri na wewe ulifika na barabara hiyo sasa imeamza kujengwa, lakini ahadi ilikuwa ni ujenzi wa kiwango cha lami; je ni lini sasa barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kyombo, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilikuwa inafunguliwa na tumeishaifungua na baada ya kuifungua hatua inayofuata nikufanya upembuzi na usanifu na ndiyo tunavyoelekezwa na ilani kwamba barabara zote ziwe kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hiyo barabara itafanyiwa upembuzi na usanifu wa kina kadri fedha itakavyokuwa inapatikana, ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kuhusu ujenzi wa barabara ya Morogoro - Njombe boarder Serikali imedhamiria kujenga kilometa 100 kwa maana ya lot one na lot two.

Swali naomba Serikali ithibitishie Wananchi wa Mrimba je, ni lini hizi kilometa 100 kwa lot zote hizi mbili zitaanza kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunavyosema sasa hivi zabuni zimeishaandaliwa na tuko kwenye hatua za mwisho kutangaza hizo lot mbili ambayo ndiyo barabara inayokwenda kuunganisha na barabara ya Kibena - Madeke, ahsante. (Makofi)
MHE. ASK. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa Mheshimiwa Rais alipofika Bunju B, aliahidi kwamba barabara ya Bunju B kupitia Mabwepande itajengwa kwa kiwango cha lami; je, unaweza kuwahakikishia wananchi wa Mabwepande kwamba itawekwa kwenye bajeti ijayo 2022/2023?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Gwajima, Mbunge wa Kawe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri na mimi nimeitembelea hii barabara na kama alivyoomba iwepo kwenye bajeti Bunge hili ndiyo litaamua hiyo barabara ipitishwe kuwa kwenye bajeti, lakini sisi kama Wizara tunategemea kuipendekeza iwepo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami kwa kuwa pia ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, ahsante.
MHE. AGNESS E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante; ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami kipande cha barabara kutoka Masasi kwenda Nachingwea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hokororo, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi - Nachingwea kilometa 45 imepangiwa bajeti kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, lakini pia kipande cha Masasi - Nachingwea hadi Liwale pia kimeingizwa kwenye Mpango wa EPC+F ambapo wakandarasi tayari wameishaoneshwa barabara hiyo na tayari tunategemea pengine kufungua zabuni kipindi si kirefu, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na mpango wa Serikali wa kujenga barabara ya bypass kuanzia Kata ya Kisaki - Unyamikumbi - Unyambwa mpaka Mtipa na feasibility study imeshafanyika; nataka kujua tu commitment ya Serikali ni lini ujenzi huu utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema usanifu umeishakamilika, sasa hivi Serikali inatafuta fedha ili tuweze kuanza kujenga kipande hicho cha bypass, ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri, kwani barabara hii ni muhimu sana kwa wananchi wa Jimbo la Nyamagana na Jiji la Mwanza kwa ujumla, ukizingatia kwa sasa tuna mradi mkubwa wa daraja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na upembuzi yakinifu unaokamilika mwezi huu, naomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie kwamba baada ya upembezi yakinifu kukamilika na bajeti itakuwa imeshaanza, kwenye mapitio ya bajeti, Serikali itakuwa tayari kuhakikisha barabara hii inaingia kwenye mpango na kuanza kujengwa upya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, Mbunge wa Nyamagana kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mwezi huu wa Nne tarehe 27 tutakamilisha usanifu wa kina. Kama alivyoomba kwamba baada ya kukamilika Serikali itafanya nini kwenye mid review ya bajeti ya Wizara?

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali imesikia ombi lake, nasi tunajua msongamano wa barabara hiyo. Tumelichukua na tutaangalia jinsi ya kufanya pale itakapokamilika na kujua gharama ya barabara hii. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. barabara Kolandoto - Munze - Mwangungo yenye kilometa 63 ni barabara ambayo imo katika mpango wa Ilani ya Utekelezaji ya Chama cha Mapinduzi na pia ipo katika mpango wa bajeti ya 2021/2022: Ni lini utekelezaji wa mradi huu utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara Kolandoto - Mwangungo kwenda Lalago ni barabara ambayo iko kwenye ilani na imekuwa ikipangiwa bajeti. Barabara hii ni ndefu inayokwenda mpaka Sibiti - Mbulu, kwa maana ya Hyadom – Mbulu. Barabara hii imeanza kutekelezwa kwa vipande na kwa sasa tutaanza ujenzi wa kipande cha Mbulu – Hyadom kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2020, wakati anafunga kampeni za uchaguzi katika Jimbo la Ushetu, alipokea simu kutoka kwa aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati Dkt. Magufuli na akawaahidi maelefu ya wananchi pale kwamba atawajengea kilometa 54 za lami kutoka Kahama – Nyandekwa - Iboja mpaka Iyogo kilometa 54 za lami: je, ahadi hii itaanza kutekelezwa lini kwa wananchi wa Ushetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumekuwa tukisema, ahadi zote za viongozi wa Kitaifa ni ahadi ambazo zinatekelezwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara zote ambazo zimeahidiwa tunazo lakini tunaendelea kuzitekeleza kadri ya upatikanaji wa fedha ikiwa ni pamoja na hii barabara ambayo Mheshimiwa Rais aliahidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii pia itajengwa kwa kiwango cha lami kama ambavyo Mheshimiwa Rais aliagiza. Ahsante. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ipo dhamira ya Serikali ya kuunganisha mikoa yote kwa barabara za lami. Mkoa wa Singida ni miongoni ni mwa mikoa ambayo haijaunganishwa na mikoa mingine ukiwemo Mkoa wa Simiyu na Mkoa wa Mbeya.

Je, dhamira ya Serikali ya kujenga barabara ya Mkiwa – Itigi – Rungwa hadi Makongorosi imefikia wapi kuanza kujengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Massare, Mbunge wa Itigi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni barabara kuu ambayo inatoka Mkiwa – Itigi - Rungwa hadi Makongorosi – Chunya. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ni kati ya barabara 22 ambazo ziko kwenye maandalizi ya kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami kuanzia Mkiwa kwenda Manyoni mwaka huu wa fedha kilometa 50. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Barabara ya kutoka Newala kuelekea Masasi kupitia Mitesa imechukua muda mrefu sana kuanza licha ya kwamba fedha ipo, kwa nini barabara hii imechukua muda mrefu kiasi hiki? Lini barabara hii itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nimemsikia vizuri, anaongelea barabara ya Newala kwenda Masasi kuanzia Munivata. Barabara hii ilishapatiwa fedha na ipo kwenye maandalizi ya kuanza ujenzi wa kiwango cha lami. Kwa hiyo, suala tu ni kwamba, mikataba tayari inaandaliwa kwa ajili ya kuanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kuanzia Mnivata, Newala hadi Masasi yenye urefu wa kilometa 160 kama nimemwelewa vizuri.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nami napenda kujua ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha njia nne barabara kuu ya TANZAM, kipande cha Uyole mpaka Songwe kupitia Mbeya Jiji na Mbalizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Jiji la Mbeya ni kati ya majiji ambayo yana changamoto kubwa sana ya usafiri katika kipindi hiki; na Serikali ina njia mbili ya kutatua changamoto hizi. Moja, ni kujenga bypass ya kuanzia Uyole hadi Songwe yenye urefu wa kilomita 49; na pia kupanua barabara inayopita katikati kutoka njia mbili kwenda njia nne.

Mheshimiwa Spika, hatua ya haraka ambayo Serikali imechukua ni kupanua kwanza njia mbili kwenda njia nne kuanzia Uyole hadi Songwe eneo la Ifisi kilomita 29 na taratibu za manunuzi zinaendelea hadi tunavyoongea hapa sasa kwa mwaka huu wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa kuwa barabara kuu ya Makambako – Songea inayopitia katika Mji wa Njombe imezidiwa na inahitaji ukarabati mkubwa: Je, ni lini barabara hii sasa itaanza kukarabatiwa au kujengwa upya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara aliyoitaja ambayo inaanza Makambako, Njombe hadi Songea ni kati ya barabara za zamani sana kujengwa miaka ya 1984. Tayari usanifu ulishakamilika na Serikali inaongea na Word Bank ili tuweze kupata fedha kwa ajili ya kuikarabati barabara hii. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tayari ipo kwenye mchakato wa kuongea na hizi taasisi za kibenki kwa maana ya kifedha ili tukishafanikiwa basi ukarabati wa barabara hii uanze.
MHE. PHILLIPO A. MULUGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ujenzi wa barabara ya lami kutoka Mbalizi mpaka Mkwajuni, upembuzi yakinifu na usanifu umekamilika na mwaka huu wa fedha Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha, aliniahidi kwamba mwaka 2022/2023 watatenga fedha kwa ajili ya kukamilisha barabara hiyo lami. Je, anakumbuka; na kwamba tayari mwaka huu wameshatenga fedha za barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mulugo, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba ni dhamira ya Serikali kujenga barabara zote kwa kiwango cha lami na hasa zile zinazounganisha mikoa na mikoa, wilaya na wilaya lakini pia barabara kuu na barabara muhimu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya Serikali bado iko pale pale. Isipokuwa barabara ipi inaanza, inategemea kimsingi na bajeti ama na fedha itakayokuwa imepatikana kuanza ujenzi.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, dhamira Serikali bado iko pale pale kujenga barabara hizi kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na barabara ya Mheshimiwa Mulugo ambayo ameisema. Ahsante. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya Airport – Banana, Gongolamboto – Pugu - Chanika ndiyo barabara pekee kwenye Mkoa wa Dar es Salaam ambayo siyo double road. Naomba kujua mpango wa Serikali wa kuipanua barabara hii na kuwa ya njia nne.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya kuazia Airport kwenda Gongolamboto ni sehemu ya barabara ya Nyerere Road. Barabara hii kama nimemwelewa Mheshimiwa Mbunge, ni barabara ambayo ipo kwenye awamu ya tatu ya hizi barabara za kwenda kwa kasi kwa maana ya BRT. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mkataba umeshasainiwa tarehe 17 Machi na Mkandarasi atakayejenga pale ni Sinohydro.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunategemea muda wowote kuanzia pale katikati ya mji kwenda Gongolamboto barabara hii itaanza kujengwa kwa maana ya kupunguza msongamano kwa wananchi wa Dar es Salaam, hasa kwenye Jimbo la Mheshimiwa Silaa, Ukonga. Ahsante.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara ya Tegeta – Bagamoyo imejengwa na TANROADS na kuna sehemu ambayo hawajaweka mitaro kabisa, inasababisha mafuriko katika maeneo ya Basihaya na Tegeta: -

Mheshimiwa Spika, ni nini tamko la Wizara juu ya ku-repair eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kawe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala aliloliongelea la kusababisha mafuriko kwa sababu ya ujenzi wake kwa sababu ya barabara zimeinuka, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumelichukua na ninaomba kutumia nafasi hii nimwagize Meneja wa Barabara wa Dar es Salaam aende akafanye study ya nini Wizara tufanye ili tuweze kuondoa changamoto hii kwa wananchi. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami barabara inayotoka Kahama - Geita? Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri anipe majibu ya kweli, barabara hii imekuwa ni kero ya muda mrefu.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kahama – Ilogi kwenda Geita ni barabara ambayo inauganisha mikoa miwili; Mkoa wa Shinyanga na Mkoa wa Geita kupitia kwenye Jimbo la Mheshimiwa Iddi ambao ni Jimbo la Msalala.

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii ni barabara ya kiuchumi na Serikali tumefanya majadiliano na wenzetu wa Barrick, lakini imeonekana bado wanasitasita kuanza kujenga hii barabara.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii sasa Serikali itaichukua ili ione namna ya kuifanya na pengine katika bajeti tunayoendelea kuiendea pengine tutaona nini cha kufanya ili tuanze kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii niulize swali la nyongeza. Barabara ya Tabora – Ulyankulu imekuwa sasa ni muda mrefu zaidi ya takribani miaka kumi imejengwa kilometa mbili tu za lami. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mkakati gani sasa wa kuhakikisha barabara hiyo ya muda mrefu inakwisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Munde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa Serikali imeshaonyesha nia na kama nilivyosema kwenye baadhi ya majibu yangu kwamba dhamira ya Serikali ni kuzijenga hizi barabara na tumeshaanza, lakini kuikamilisha barabara hii kwa kweli lazima tuseme itategemea na upatikanaji wa fedha. Pale fedha itakapopatikana basi Mheshimiwa Mbunge hii barabara tutaikamilisha kwa kiwango cha lami kama tulivyoahidi na kama tulivyoanza kujenga hizo kilometa za awali. Ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pia nashukuru kwa majibu ya Serikali kwamba imejiandaa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa bypass, hata hivyo nina maswali ya nyonge. La kwanza, je, ni lini wananchi ambao wanakaa Uyole mpaka Ifisi watalipwa fidia zao ili kupisha ujenzi wa barabara hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, naomba kwa uzito wake, kuanzia Uyole mpaka Mbeya Mjini mpaka kufika airport ile barabara haina hata service road kwa maana hiyo mabasi, bajaji, maguta, malori pamoja na ambulance ambazo zinapeleka wagonjwa wa rufaa Mbeya, lakini usiombe kama unakwenda airport unaweza ukapaki gari pembeni ukapanda bajaji ama bodaboda ili kuwahi kule inakuwa shughuli.

Je, ni lini Serikali itatafuta Mkandarasi kwa haraka ili kuweza kuepusha ajali zinazotokea mara kwa mara kwa ufinyu wa barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na suala la fidia kabla ya kuanza ujenzi wa barabara hii, fidia italipwa kwa wananchi ambao watapisha ujenzi huu. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jiji la Mbeya kwamba Serikali italipa fidia kabla ya kuanza ujenzi wa barabara hii.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge lakini pia na Mheshimiwa Spika ambaye najua hili jiji ni jiji lako kwamba, ni kweli barabara hii ambayo Serikali imeamua kuchukua hatua za haraka sana kulingana na ukweli kwamba msongamano ni mkubwa.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba hatuna barabara hizi za kupaki bajaji na pikipiki lakini pia tunatambua kwamba barabara hii ndio inayopitisha mizigo karibu asilimia zaidi ya 50 ya mizigo inayotoka Bandari ya Dar es Salaam kwenda DRC, Zambia na Malawi na ndio maana Serikali imechukua jitihada na hatua za haraka kuhakikisha kwamba barabara hii inapanuliwa na wakati inafanya design ni pamoja na kutengeneza hayo maeneo ambayo yatakuwa ni ya kupaki malori, mabasi na bajaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hii itafanyika na tayari tupo kwenye hatua za manunuzi ili tunavyoanza tu Julai kazi ianze ya ujenzi huu pamoja na hizo parking ambazo Mheshimiwa Mbunge amezisema. Kwa hiyo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge hivyo. Ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, siku ya Jumanne liliulizwa swali la nyongeza la kuhusu hii barabara na majibu yako yalisema, ujenzi unaanza mwaka huu wa fedha ambao ni 2021/2022, majibu ya msingi hapa yanaonesha kwamba katika mwaka wa fedha 2022/2023, Sasa kwa sababu hapa umenitaja nimeona uliweke vizuri hilo tuwe tunajua 2021/2022 au 2022/2023. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba niliweke vizuri suala hili. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, tutaanza ujenzi kwa maana ya kupeleka mkandarasi site mara tunapoanza mwezi Julai, utekelezaji wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye jibu la msingi tunasema taratibu za manunuzi zimeshaanza kwa maana ya kutafuta Mkandarasi, kusaini zabuni na kuanza kufanya tathmini. Kwa hiyo, ujenzi tunasema tayari tumeshaanza kwa sababu hizo hatua zimeanza na kwamba tutakapoanza tu mwaka mpya Mkandarasi anakuwa yupo site. Lakini taratibu za manunuzi zimeshaanza na tayari tumeshatangaza. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara ya Kona ya Kiseriani ambayo inaungana na barabara ya Arusha bypass imekuwa kero kubwa sana na kusababisha msongamano wa magari katika Jiji la Arusha. Tumeona Mkandarasi amepatikana na muda wa kujiandaa umekwisha.

Je, ni lini sasa mkandarasi ataanza kazi ya kujenga barabara hii katika Jiji la Arusha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara zote za bypass lakini barabara zote za Mji wa Arusha, ziko kwenye mpango wa kujengwa. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ziko kwenye taratibu mbalimbali za manunuzi ikiwa ni pamoja na barabara ya Arusha kwenda Kisongo, Arusha kwenda Usa River, lakini pia na barabara ambayo inaunganisha barabara ya Bypass ya Arusha Kusini ambayo inaunganisha Tengeru kwenda Usa River. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zinaendelea za kuzijenga hizo barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza Serikali ni lini itaanza kujenga barabara yetu ya Bigwa
– Kisaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Taletale Mbunge wa Morogoro Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Bigwa – Kisaki ni kati ya barabara 22 ambazo ziko kwenye taratibu mbalimbali za manunuzi ili ujenzi wa barabara hii muhimu ya kutoka Bigwa – Kisaki, kwenda Bwawa la Nyerere uanze. Kwa hiyo, muda wowote taratibu zikikamilika, barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali moja. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Babati, Galapo hadi Orkesumet kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Sillo, Mbunge wa Babati Vijiji, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni barabara muhimu ambayo tayari imeshakamilishwa kufanyiwa usanifu wa kina na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, mara Serikali itakapopata fedha, barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM M. NYOKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Majengo, Ruvuma, Subira kwenda Mpitimbi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Nyoka, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Ruvuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya kazi ya usanifu wa kina ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPHAT N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, eneo la Mlowo mpaka Vwawa kumekuwa na msongamano mkubwa sana wa magari na hasa malori ya mizigo yanayopitia pale Tunduma na kuelekea huku sehemu mbalimbali, na barabara hii ambayo tunaisema ya kuanzia Mahenje, Ndolezi, Hasamba inaweza ikangezewa upembuzi yakinifu katika eneo la Ilyika, kwenda kule Kilima Mpimbi mpaka hadi pale Iboya na ikawa ni bypass.

Je, Serikali iko tayari sasa kuongeza hicho kipande kilichobaki kwa ajili ya kufanya usanifu wa kina na kuhakikisha kwamba inakuwa ni bypass? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali pili, kwa kuwa sasa wanajenga hizo mita 800 mpaka hadi pale karibu na hospitali ya Mkoa wa Songwe.

Je, Serikali itakuwa tayari katika mwaka ujao wa bajeti huu ambao tunaujadili kutenga tena kiasi fulani cha fedha kwa ajili ya kujenga kutoka pale kwenda Hasamba mpaka Ndolezi kwenye kimondo ili kusudi watalii mbalimbali waweze kufika katika eneo la Kimondo?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hasunga, Mbunge wa Vwawa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara ya kutoka Mlowo hadi Tunduma kumekuwa na msongamano mkubwa wa magari. Kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, tunafanya usanifu kuanzia Mahenje, Hasamba hadi Vwawa, sasa swali alilolitoa la kutoka Mahenje Vwawa na kufanya bypass hadi Iboya ni barabara ambayo kimsingi kwa sasa haiku chini ya TANROAD lakini wazo hilo kwa maana ya kupunguza msongamano kupita Wilaya ya Vwawa, Serikali imelichukua na italiangalia namna ya kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoisema ya kuendeleza ni utaratibu wa kuendelea na ndiyo maana tumesema tutakwenda kwa awamu. Kwa hiyo, tunauhakika kwamba katika bajeti inayokuja, baada ya kukamilisha hizo mita 800 tutaendelea na lengo ikiwa ni kukamilisha barabara zima ambayo sasa tunafanyia usanifu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami, barabara inayounganisha Mkoa wa Lindi na Mtwara, RuangWa – Nachingwea - Masasi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mpango wa Serikali kuijenga barabara ya Masasi -Nachingwea kwa kiwango cha lami, lakini itaanza tu pale ambapo Serikali itakuwa imeshapata fedha kwani tayari usanifu wa kina ulishakimilika, kwa hiyo kinachosubiriwa ni upatikana wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ujenzi wa barabara ya Loliondo - Mto wa Umbu, kipande cha Wasso - Sale umeshakamilika kwa kiwango cha lami. Nilitaka kufahamu, je, ni lini Serikali itaanza awamu ya pili ya ujenzi huu ambao ni Sale-Ngarisero.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imekuwa kero sana kwa kazi wa Ngorongoro, hasa Tarafa ya Loliondo na Tarafa ya Sale. Kwa hiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri anapokuja kunijibu naomba anipe la uhakika na linaloeleweka. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Magige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Mto wa Umbu, Loliondo, Sale, hadi Wasso, kipande cha Sale Wasso kimeshakamilika na kipande cha Loliondo kuja Ngarisero kiko kwenye mpango wa kujengwa. Lengo ni kukamilisha barabara yote ambayo ni muhimu sana siyo tu kwa wananchi wa Loliondo lakini kwa shughuli pia za utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya foleni pamoja na msongamano wa magari kuanzia eneo la Mpemba, Sogea mpaka unafika Custom Tunduma. Naomba kufahamu Serikali imejipangaje kutuondolea adha hiyo wananchi wa Mkoa wa Songwe kwa kutujengea barabara kutoka Mbozi, kwa maana ya pale Mlowo mpaka kufika Tunduma?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum Songwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ni sehemu tu ya barabara ya Igawa, Mbeya hadi Tunduma, maeneo yote haya yameshafanyiwa usanifu na yale maeneo ya Miji, barabara hizi zitajengwa njia nne ili kupunguza msongamano wa katika maeneo ya Miji ikiwemo na hilo eneo la kuanzia Vwawa kwenda sehemu ambapo tutajenga mizani.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wa kutoka Mbagala Kokoto mpaka Kongowe ili kupisha ujenzi wa barabara hiyo ambayo umetengewa fedha katika mwaka huu wa fedha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chaurembo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Kokoto kwenda Kongowe, hawa wananchi watalipwa fidia pale ambapo barabara hii itaanza kujengwa, ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Kwasadala - Kware - Lemira Kati, kilometa 15.2 ni barabara muhimu sana inayoshusha mazao kwenye soko la Kwasadala na hatimae kuja huku Dodoma na sisi kuweza kuitumia.

Je, Serikali ni lini itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saasisha Mafuwe, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ya Kware - Lemira ni barabara muhimu sana kwa wananchi wa Hai. Hivi tunavyoongea ni kwamba Serikali inatafuta fedha ili fedha ikipatikana barabara hii ambayo siyo ndefu iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mara Serikali itakapopata fedha barabara hii ambayo inasimamiwa na TANROADS itajengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLAGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona.

Je, ni lini Serikali itaendelea na ujenzi wa barabara ya njia nne kuanzia Tengeru kwenda Holili ambayo ni sehemu ya mradi wa barabara ya Afrika Mashariki unaoanzia Sakina. Barabara hii ujenzi wake ulisimama takribani sasa hivi miaka Minne.

Je, ni lini ujenzi utaendelea kwa sababu barabara ile sasa hivi ina magari mengi sana na ajali ni nyingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii inayotoka Arusha kwenda Holili ipo kwenye mpango, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tunategemea mwaka wa fedha unaoanza kujenga kati ya Tengeru na Usa River, barabara nne, lakini daraja la Kitafu litajengwa na barabara za Moshi Mjini zitajengwa katika huu mpango. Ahsante.
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri ni lini Serikali itakarabati daraja la Kimanga ambalo linazunguka Tabata, pamoja na Kata zingine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Kamoli Mbunge wa Segerea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ukarabati wa barabara hii upo kwenye usanifu na mara usanifu utakapokamilika daraja hili litajengwa. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Ilula, Mlafu, kuelekea Kilolo ni barabara ambayo ni mbaya sana. Ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu wakulima wa kutoka Kilolo wanatataka kusafirisha mazao yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tendega Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara aliyoitaja iko katika hali mbaya lakini ni azma ya Serikali kwamba kabla ya kuanza kuijenga itaikarabati kwanza ili iweze kupitika wakati Serikali ikitafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Liwale inazo barabara moja muhimu sana, barabara ya uchumi, barabara ya Mkombozi. Barabara hii nimeizungumza mara nyingi mno, barabara ya Nangurukuru Liwale. Wananchi wa Liwale wanataka kusikia barabara hii itajengwa lini kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ilishakamilishwa kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, Mheshimiwa Kuchauka atakubaliana nami kwamba Wizara ina mpango wa kuanza kuijenga barabara hii walau kwa awamu mwaka wa fedha unaokuja. Kwa hiyo, itategemea sana na upatikanaji wa fedha, lakini Serikali ina mpango kuianza kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumuuliza Naibu Waziri kwamba kwa kuwa barabara nyingi zilizoko chini ya TARURA, mifereji yake imejaa takataka, imeota majani na ni nyingi na hasa zile Mjini. Na kwa kuwa, tunajua kwamba TARURA ina upungufu wa wafanyakazi: -

Je, Serikali haioni ni muhimu wakaishauri TARURA iingie mkataba agencies yoyote ambayo inaweza kusaidia kufanya usafi wa barabara hizi?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, wazo tumelipokea, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zipo taratibu wa barabara hizi kufanyiwa usafi. Usafi ni pamoja na kufyeka, kuondoa mchanga, ama kuzibua makaravati yanayokuwa yameziba, kazi hizi huwa zinatangazwa ambapo Wakandarasi wanaomba na kupewa hizo Kandarasi kwa ajili ya kufanya huo usafi. Kwa hiyo utaratibu upo na barabara hizo zinasafishwa kwa upande wa TARURA TAMISEMI wanasimamia kuhakikisha kwamba barabara zinasafishwa lakini kwa barabara za TANROADS ambazo zipo chini ya Wizara ya Ujenzi pia zinasimamiwa kuhakikisha kwamba barabara hizi hazizibi kwa sababu ya uchafu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nitoe rai kwa watumiaji wa barabara kwamba sehemu kubwa ya kuziba hii barabara na uchafu wakati fulani ni kwa sababu ya kazi za kibinadamu ambazo watu wanafanya kazi kwenye hifadhi ya barabara na kusababisha tatizo hilo. Kwa hiyo, niwaombe wananchi kupitia nafasi hii kutokufanya kazi za maendeleo kwenye hifadhi za barabara kwa sababu zinazababisha barabara hizo kuziba. Ahsante. (Makofi)
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu ya Serikali lakini tangu 2017 mpaka sasa ni miaka mitano hakuna kinachoendelea. Swali la kwanza, nataka commitment ya Serikali lini ujenzi wa uwanja huo ama ukarabati utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, nataka kujua mkakati wa Serikali ambao utahakikisha ujenzi huu unafanyika kwa wakati? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ramadhan Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu katika jibu la msingi, ujenzi huu utaanza pale ambapo Serikali itakuwa imepata fedha na kuupangia uwanja huu kuanza ujenzi. Kwa hiyo, commitment ya Serikali ni kwamba tayari tumeshaanza hatua za awali kwa maana ya kufanya usanifu na kama nilivyoeleza kwenye jibu la msingi, tunaendelea kutafuta fedha pamoja na Washirika wa Maendeleo ili fedha ikipatikana tuanze kuujenga huu uwanja wa Singida.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Mkoa wa Manyara ambao eneo lilishatengwa eneo la Mwada?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, taratibu zinaendelea za kutwaa eneo ambalo uwanja huu utajengwa na baada ya taratibu hizo kukamilika uwanja huu utaanza kujengwa.
MHE. HAJI MAKAME MLENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali hata hivyo na maswali mawili ya nyongeza.

Je, Wizara yako inayo mpango wowote wa kutengeneza bustani kando kando ya barabara hasa maeneo ya Mjini?

Swali la Pili, kwa kuwa mazingira ni muhimu. Je, Wizara yako inashirikiana vipi na Wizara ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira katika kuratibu mazingira, hasa bustani katika maeneo ya pembeni ya barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Makame Mlenge Haji, Mbungwe wa Chwaka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria na Kanuni zimetoa maelekezo kwa watu wote ambao wanataka kutumia hifadhi ya barabara bila kuathiri matumizi wafike kwenye mamlaka husika ili waweze kuendeleza na kupendezesha Miji. Suala hili linafanyika kwa barabara za TANROADS, vilevile barabara za TARURA kwa maana ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuhusu kushirikiana na hifadhi ya mazingira ni kwamba taratibu na sheria inayoongoza iko chini ya Wizara ya Ujenzi. Kwa hiyo, tunahakikisha kwamba tukishampa mtu kazi, kwa maana ya kumpa kibali, basi anafanya kazi kulingana na miongozo na taratibu ambazo zimewekwa kwa mujibu wa Sheria na Kanuni ambayo inalinda kutumia hifadhi ya barabara. Ahsante.
MHE. ALAUDIN H. SALIM : Mhesnimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na kwamba Wilaya ya Ulanga ni kitovu cha uchimbaji wa madini, lakini pia kuna miradi mikubwa ambayo inaenda kuanza ya madini ya kinywa ambayo ina manufaa makubwa kwa nchi lakini pi kwa uchumi wa wananchi wa Wilaya ya Ulanga. Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 67 kwa kiwango cha lami?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Tarafa ya Mwaya ni tarafa inayoongoza kwa kilimo cha pamba pamoja na ufuta.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili wanachi hawa waweze kufikisha mazao yao sokoni kwa urahisi zaidi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika,naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Alaudini Hasham Salimu Mbunge wa ulanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa Serikali ni kujenga barabara kwa kiwango cha lami. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa barabara ambazo zinarudiwa na TANROAD kutoka Mpilo – Mahenge iko kwenye mpango wa EPC+F na tayari Wakandarasi wameshapita na barabara aliyoitaja ya pili Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kuijenga kwa kiwango cha lami ili kurahisisha usafiri na kuwafanya wananchi wa Ulanga waweze kufanya biashara zao kwa urahisi. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua ni lini ujenzi wa kipande cha barabara kutoka Mbande - Kisewe mpaka Msongola utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chaurembo Mbunge wa Mbagala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja iko kwenye mpango na tunategemea utekelezaji utaanza mwaka huu wa bajeti.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, barabara ya USA River kwenda Oldonyo Sambu kwa kupitia Hifadhi ya Arusha imejengwa kwa kiwango cha lami hadi Getini Ngongongare.

Je, ni lini Serikali itaendelea na ujenzi wa barabara hii kutoka ngare na nyuki Kwenda Oldonyo Sambu na kuunganisha Barabara ya Kwenda Namanga na Moshi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye ilani na Mpango wa Serikali ni kuijenga kwa kiwango cha lami barabara aliyoitaja. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa jimbo lake kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuijenga barabara hiyo.
MHE. ENG. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Haidong - katesh imeshatengewa milkioni 300 kwa ajili ya ujenzi na milioni 280 kwa ajili ya usanifu wa kina. Je, Serikali ina mpango gani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pilli, Barabara ya Nangwa – Kondoa ina daraja ambalo limekuwa likikwamisha wananchi, daraja la Munguli, ilitengewa milioni 600. Je, ujenzi wake utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Xaday, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Hydom – Katesh ipo kwenye mpango na imepangiwa fedha. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa utekelezaji ni mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, Daraja la Munguli linalounganisha Kondoa na Hanang pia limetengewa fedha kwa ajili ya kulijenga Mwaka huu wa fedha. Ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa TANROADS Mkoa wa Iringa walitii agizo la kwenda kuangalia barabara ya Mchepuko wa Mlima Kitonga, na tayari wameshafanya maandalizi ya awali. Je, Serikali inasemaje kuhusu kuanza usanifu na kuijenga barabara hiyo ya Mchepuko wa Mlima Kitonga ili wananchi waweze kupita kwa urahisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyokiri kwamba tayari tumeshatoa maelekezo na baada ya kuipitia barabara sasa kinachofuata ni kuanza kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, suala hilo litafanyika kwa sababu ndiyo barabara itakayotuokoa ikitokea changamoto yoyote katika Mlima kitonga. Ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, Barabara hii ya Fulo kupitia Nyambiti mpaka Malya ni barabara ya muhimu sana kwenye uchumi wa Serengeti ya Kusini, na ni barabara ambayo Serikali imekuwa ikiahidi kuendelea kutafuta pesa, wakati huo Serikali ikitambua Jimbo la Sumve hatuna hata milimita moja ya lami.

Je, ni lini sasa seriously pesa hizi zitapatikana, mkafanya upembuzi yakinifu na kuanza kuijenga barabara hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara yenye urefu wa kilometa 71 inayotokea Magu inapita Bukwimba – Nkalalo – Ngudu mpaka Hungumalwa nimekuwa nikiiombea kila mara ijengwe kwa kiwango cha lami na Serikali mlijibu kwamba sasa mmejipanga kuijenga katika bajeti hii.

Je, sasa ni lini ujenzi huo unaanza au inaendelea kupewa ahadi kama ambavyo imekuwa kawaida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kasalali Emmanuel Mageni, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakubaliana naye, barabara hii bado haijafanyiwa usanifu ; na nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna barabara mbili tu ambazo zilikuwa bado hazijafanyiwa usanifu katika Mkoa wa mwanza ikiwepo hii. Tumeshamwagiza Meneja wa Mkoa aangalie kama kutatokea saving yeyote kwenye hela ya maendeleo, hii barabara tuanze. Tukuhakikishie barabara hii lazima itafanyiwa usanifu katika kipindi cha mwaka wa bajeti huu tunaokwenda na mpango wa sasa.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, barabara ya Hungumalwa hadi Magu, Mheshimiwa Mbunge nishahidi, Waziri ameongea naye na tumeshaahidi. Tayari Meneja wa Mkoa ameelekezwa aitangaze kuianza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi ya swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Kiranjeranje – Nanjirinji mpaka Ruangwa imefanyiwa upembuzi wa kina na upembuzi yakinifu kwa lengo ya kujengwa kwa kiwango cha lami. Wakati Wana-Nanjirinji tukisubiri lami, hali ya barabara hii si nzuri, hususan maeneo kutoka Mangaja – Nakiu – Nanjirinji mpaka Ruangwa, je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kutoa maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Lindi ili wakakagua barabara hii na wafanye utaratibu wa dharura?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilifanyiwa usanifu wa awali, na mwaka huu tunakamilisha usanifu wa kina. Kwa hali aliyoelezea nataka tu nitumie fursa hii kumuagiza meneja wa TANROADS aende aiangalie hiyo barabara na kama kutakuwa na changamoto kubwa inayohitaji msaada wa Wizara basi tuweze kuwasiliana; lakini tunavyoongea leo aende aitembelee hiyo barabara ili aweze kurekebisha na wananchi waendelee na shughuli zao za kawaida. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona niulize swali la nyongeza. Pamoja na nia njema ya Serikali kupeleka miradi ya barabara za lami kwenye Jimbo la Kibamba hata hivyo pamekuwa na sintofahamu ya miradi hiyo kutobeba components za fidia zaidi ya migogoro na wananchi. Je, Serikali inasema nini juu ya jambo hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE: Mheshimiwa Spika, naomba nimwombe Mheshimiwa Issa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, aweze kuwasilisha swali kama swali kwa maana ya masuala ya fidia. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali, ni lini sasa barabara inayotoka Chang’ombe kupitia DUCE mpaka Mgulani mtamalizia, kwa sababu sasa hivi malori ni mengi sana ambayo yanapeleka vifaa viwandani na njia haipitiki sasa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, labda tu nichukue nafasi hii kumuhimiza mkandarisi lakini pia na Meneja wa TANROADS kuhakikisha kwamba barabara hii inakamilishwa haraka. Mheshimiwa Mbunge kama kutakuwa na changamoto ya ziada naomba tuonane nae ili tuweze kutatua hiyo changamoto kama ipo kwa upande usimamizi ama kwa mkandarasi mwenyewe. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Barabara ya kilometa zaidi ya 300 ambayo inatoka Lumecha Kupitia Msindo – Mputa – Kitanda mpaka Londo kwa Mpepo Morogoro, imefanyiwa Upembuzi na usanifu wa kina kwa muda mrefu sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami kwa haraka sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya inayoanzia Lumecha- Kilosa kwa Mpepo, Malinyi hadi Ifakara kama alivyoisema, tumejibu mara kwa mara kwamba imeingizwa kwenye mpango wa EPC+F, na hivi tunavyoongea wakandarasi wameshaoneshwa hizo barabara na wako wanaandaa zabuni kwa ajili ya kuijenga kwa mfumo huo wa EPC+F, ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri. Wananchi wangu wa Mitesa Namalenga, Mdibwa, Nagaga, Chungutwa pamoja na Mpeta, wote hawa wamekuwa wakitarajia ujenzi. Sasa, kwa niaba yao nauliza, ni lini ujenzi huu utaanza?

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kuhusu fidia, nimemsikia amejibu kwamba fidia imeanza, namuomba Waziri anijibu kwa asilimia ngapi jibu hili lina ukweli? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa vijiji vyote alivyovitaja kwamba barabara hii itajengwa. Tulishatangaza na tumesema tumefungua; na kwa kuwa inafadhiliwa na African Development Bank, mchakato wa manunuzi tuna uhakika by March barabara hii itaanza kujengwa, japo sisi tunasema tayari tumeshaanza kulipa fidia mchakato unaendelea.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa swali lake la pili, kwa asilimia ngapi, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye jimbo lake, jumatatu watakuwa hapo wanalipa fidia kwani tayari Mnivata hadi Chikwaya Wilaya ya Mtwara tayari tumeshalipa, baada ya Tandahimba itakwenda Newala na Masasi na fedha ipo tayari, ahsante. (Makofi)
MHE: EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, Serikali itaanza lini ujenzi wa kilometa 30 kwa kiwango cha changarawe kutoka Uyogo kupita Iberansua, Mbika mpaka Urowa, ambapo barabara hii imekuwa kiungo kikubwa sana kwa wananchi na uchumi wa halmashauri wa Ushetu na mpaka tunavyoongea sa hizi magari yanadondoka ya wakulima wanaosafirisha mazao yao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Nyongeza la Mheshimwa Cherehani, Mbunge wa Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii kama alivyosema inahitaji kujengwa kwa changarawe. Sehemu ya barabara hii ilikuwa chini ya barabara ya TARURA na sasa ndo imepangiwa bajeti. Nataka nimuhakikishie

Mheshimiwa Mbunge kwamba mwaka huu tutakwenda kuikarabati barabara hiyo. Nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa Mkoa wa Shinyanga aende aitembelee hii barabara na kuifanyia ukarabati wa haraka ili kuokoa maisha na mali na hayo magari ya wananchi. Ahsante.
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Barabara ya uchumi inayoanzia Mtwara Mjini kuelekea Msimbazi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shamsia Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara iliyoitajwa tayari tumeshaifanyia upembuzi wa kina, Serikali sasa inatafuta fedha kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT.CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, kwenye barabara ya Himo kuelekea Rombo, eneo wanalovuka wanafunzi wa Shule ya Korona na maeneo yale yanayokaribia masoko ya Kisambo na Mwika ni hatari sana kwa wapita njia lakini kwa magari pia. Je, Serikali ipo tayari kujenga matuta kwenye maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la matuta ni suala ambalo linategemeana na wataalam. Naomba niwaagize wataalam wa TANROADS hasa Meneja wa Mkoa wa Kilimanjaro, aende akafanye usanifu ili aone kama kuna umuhimu wa kufanya suala hilo. Ni vyema akawasiliana na Mheshimiwa Mbunge ili aone maeneo ambayo anahitaji suala hili linakotakiwa kufanyika, ahsante.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya Mtoni - Bombo kwenda mpaka Bashewa, na barabara hiyo hiyo kutokea upande wa Maramba mpaka Tanga, usanifu wake lini utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dunstan Kitandula, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni barabara ambayo tumeitengea fedha kwa ajili ya kukamilisha usanifu wa kina mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, nina uhakika barabara hii mwaka huu itaanza kufanyiwa usanifu wa kina. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ni nini kinakwamisha ujenzi wa barabara kipande cha Haydom mpaka Labay?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hakuna kinachokwamisha ujenzi wa barabara hii. Zabuni ya kwanza ilitangazwa kilometa 25 ambayo inatoka Mbulu Mjini hadi Galbad; na kuanzia Labay - Haydom, barabara hii zabuni za kuitangaza zinaendelea. Kwa hiyo, awe na Subira, zikikamilika taratibu za manunuzi, barabara hii itatangazwa kwa kilometa nyingine 25 lakini pia barabara hii imeingizwa kwenye EPC+F. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Kinyanambo C - Mapanda hadi Kisusa katika Jimbo la Mufindi Kaskazini? Maana ilikuwa imeahidi kujenga kilometa tano tano na ni barabara ya kiuchumi.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja itajengwa kwa kiwango cha lami kufuatana na upatikanaji wa bajeti. Kwa hiyo, Serikali itaendelea kutafuta fedha kuijenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, naomba kufahamu barabara ya kutoka uwanja mdogo wa Airport Arusha mpaka eneo la Kilombero kwa kiwango cha njia nne utaanza lini; na hasa ukizingatia kwamba barabara hii ikikamilika itasaidia kuondoa msongamano na changamoto ya mafuriko kwenye Kata za Ungalimitedi, Sombetini na Usunyai?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Airport kwenda Kilombero ni barabara ya muhimu kwenda njia nne; na ujenzi wa barabara hii kama ilivyo kwenye Majiji mengine utategemea sana upatikanaji wa fedha. Nadhani labda kwenye mpango huu tunaouendea, basi tutaomba tuweze kuanza kuweka mpango wa kuijenga barabara hii kwa kiwango cha barabara nne ili kupunguza msongamano katika Mji wa Arusha. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa jibu la Serikali la mara zote ni kuendelea kutafuta fedha kwa ajili ya utengenezaji wa barabara hizo zilizotajwa lakini kwa kuwa pale ni eneo muhimu na kuna ajali nyingi zinatokea. Je, Serikali haioni kwamba tunaweza kutanua maeneo yale kama ambavyo imetanuliwa barabara ya pale Picha ya Ndege, Kongowe na Chalinze ili kuweza kupunguza msongamano wa eneo lile la Mlandizi?

Mheshimiwa spika, swali la pili, kama tatizo ni fedha na barabara hii inayozunguzwa, amezungumza barabara ndefu na mimi shida yangu ni pale Mlandizi, hatuwezi kuweka taa za haraka barabarani za kuongozea magari ili kupunguza misongamano iliyopo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwakamo, Mbunge wa Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge wa Kibaha na sote ni mashahidi ambao wengi tunapita kwenye barabara hii. Kutokana na hoja ya Mheshimiwa Mbunge na jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia ni kweli tulichosema ndio mpango wetu wa Wizara, lakini Wizara baada ya kufuatilia tunajaribu kuangalia uwezekano, tutafanya study tuwe na mpango wa muda mfupi ili kupunguza ajali, lakini pia na msongamano.

Kwa hiyo tutaangalia kama njia sahihi na rahisi itakuwa ni kupanua barabara kwa maana ya njia nne kama sehemu nyingine ama kuweka taa ili kwanza kuokoa ajali, lakini pia kupunguza msongamano ambao sasa umekuwa ni adha kubwa kwenye hiyo barabara. Msongamano huo pia upo hasa katika hizi njia ndogo zinazotoka Bagamoyo kwenda Mzenga ambapo wananchi wengi sana wanachelewa kukatisha ile barabara na kuona magari makubwa tu ndio yanayopita kwa muda mrefu. Kwa hiyo, tumelichukua na Wizara tunachukua kwa umuhimu mkubwa ili kuokoa ajali na pia kupunguza msongamano. Ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kilomita 25 kwa kiwango cha lami katika maingilio ya Daraja la Sibiti kwa kuwa bajeti yake imetengwa mwaka huu wa bajeti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunategemea kujenga barabara za maingilio zenye urefu wa kilometa alizozitaja kama 23. Barabara imeshakamilika na tuko mbioni kwa muda wowote tutakapokuwa tumekamilisha fedha kwa sababu tunaendelea na hiyo mipango ya kuhakikisha kwamba maingilio yale yanajengwa kwa kiwago cha lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango upo, tumeahidi na tutautekeleza kadri fedha zitakapopatikana, kama si mwaka huu basi mwaka wa fedha tutakaouanza.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa wananchi wa Makambako wana mategemeo makubwa sana katika eneo la Idofi ambako Serikali imekuwa ikiahidi kwa muda mrefu, je, ni lini watajenga one stop center na kumalizia fidia ambayo ilibaki kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Forodha cha Idofi ni kati ya vituo vingi vya Tanzania ambavyo tunategemea kuvijenga na tayari vilishaainishwa. Sasa hivi tunachofanya ni kupata fedha na kwanza kuwalipa fidia wale ambao wanapisha ujenzi na baada ya hapo tunaanza kujenga Kituo hiki cha Forodha pale idofi katika Jimbo la Makambako. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Napenda kuuliza, je, ni lini barabara ya mzunguko kwenye Manispaa ya Mororogoro kuanzia Juniour Seminary mpaka Kihonda itajengwa ili kupisha msongamano wa magari sehemu za Msamvu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum Morogoro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Dkt. Ishengoma kwa jinsia anavyofatilia ujenzi wa hii barabara ya mzunguko Morogoro. Taratibu bado zinaendelea za kufanya usanifu wa hiyo barabara ili kupunguza msongamano katika barabara kuu inayopita Msamvu kwenda Dar es Salaam. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mara usanifu utakapokamilika barabara hii itaanza kujengwa. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Je, ni lini Serikali itajenga kilometa saba kwa kiwango cha lami za barabara kati ya Nasio-Mutunguru- Masonga ili kuondoa shida zilizopo kwenye barabara ile? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hiyo aliyoainisha Nansio Mutunguru yenye urefu wa kilomita saba ipo kwenye mpango mkubwa wa kujenga barabara ya lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango bado upo, utaanza tu pale ambapo fedha tutakuwa tumeipata na ujenzi huu tutaanza na kukamilisha hizo kilomita saba za lami katika Kisiwa cha Ukerewe.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini barabara ya Utegi hadi Kilongwe inayounganisha Nchi za Tanzania na Kenya kwa upande wa Rorya itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tuna kila sababu ya kuunganisha barabara zetu za lami na nchi jirani, lakini tuna barabara za kawaida na barabara kuu. Barabara ambayo tumeunganisha na Kenya ni ile barabara kuu ambayo inatoka Tarime kwenda mpaka wa Kenya ambao tayari ni barabara ya lami. Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa barabara hii inatumika sana na wananchi wa Rorya na Watanzania kupitia Utegi kwenda Rorya, barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kadri Serikali itakapokuwa imefanya usanifu na kupata fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda wa ujenzi wa barabara hii umekwisha, je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha barabara hii inaisha haraka ili kuondoa msongamano katika Barabara ya Kilwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni lini Serikali itamalizia kwa kiwango cha lami kipande cha kilometa tano cha Mbande- Kisewe mpaka Msongora?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chaurembo Abdallah, Mbunge wa Mbagala, kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza tutahakikisha kwamba barabara ile kipande ambacho kimebaki cha kilomita tano chote tunakijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kukamilisha daraja ambalo limeshakamilika na sasa tunachoendelea ni kuweka lami pale juu kwenye daraja ambalo tunalijenga.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kufikia mwakani barabara ile yote tutakuwa tumeijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kukamilisha hilo daraja ambalo lilikuwa ni changamoto kubwa sana kwa wananchi ambao wanatumia barabara hiyo.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika,
nakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali moja la nyongeza. Ujenzi wa barabara ya mwendokasi kwenda Mbagala pamoja na magari yanayotoka bandarini na kuingia bandarini na uwepo wa mizani katika eneo la bandari linaleta usumbufu mkubwa sana kwa wakazi wa Kigamboni ambao wanatumia Daraja la Nyerere. Je ni nini mkakati wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kuhakikisha kwamba adha wanazozipata wananchi zinaondokana na changamoto hizi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Faustine Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha kwamba barabara zote na hasa za mjini zinajengwa na kupanuliwa kwa maana ya magari yaweze kupita ama mawili ama matatu ama manne. Hata hivyo, kama kuna suala ambalo liko very specific kwa barabara ambayo ameainisha Mheshimiwa Mbunge, nitamwomba tuweze kuonana naye kama Wizara ili tuone kama kuna changamoto yoyote ambayo iko tofauti sana tuweze kuwa na mpango wa haraka kuweza kuondoa changamoto hiyo kwa hiyo barabara ambayo ameainisha Mheshimiwa Mbunge.
MHE. SAMWEL X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Barabara ya Nangwa- Gisambalang-Kondoa inayotegemewa na Kata ya Gisambalang, Dirma, Simbai, Sirop na Wareta ina daraja ambalo limekatika toka mwaka 2019.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga hilo Daraja la Muguri B?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja alilolitaja ambalo liko sasa hivi kwenye usanifu na tunategemea kwenye mwaka wa fedha ujao daraja hilo lianze kujengwa. Ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Napenda kuuliza swali moja.

Ni lini barabara ya kutoka Kolandoto mpaka Meatu itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kolandoto kwenda Meatu ni kati ya barabara ambazo zimeainishwa kwenye Ilani, na pia zipo kwenye mpango wa kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kuanzia na kilometa 92. Kwa hiyo, sasa hivi kinachosubiriwa ni Serikali kupata fedha ili ujenzi wa barabara hii uanze. Ahsante. (Makofi)
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Barabara ya kutoka Kinyerezi kupitia Segerea hadi Tabata Relini ni barabara ambayo imekuwa na changamoto kwa muda mrefu; na Serikali wamekuwa wakiahidi mara kwa mara bila ya utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, napenda kufahamu kauli sahihi kuhusiana na barabara hii. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lambert, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Segerea kwenda Relini niliijibu wiki iliyopita wakati Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Segerea alipoliuliza. Nilichosema na bado naendelea kusema, barabara ilikuwa imefumuliwa na kulikuwa na changamoto ya Mkandarasi. Tunapoongea sasa hivi, Mkandarasi yupo site kukamilisha vipande vyote ambavyo vilikuwa vimefumuliwa.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hiyo barabara inaendelea kutengenezwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi hii. Kwa nyakati tofauti viongozi wetu wa kitaifa waliahidi wananchi wa Wilaya ya Misenyi kutengeneza barabara ya Mutukula kwenda Minziro, na kwa bahati nzuri Naibu Waziri alikwenda kutembelea eneo hilo, akapokelewa kwa shangwe, lakini mpaka leo barabara hii haijatengenezwa pamoja na kuingizwa kwenye bajeti.

Je, ni lini barabara hiyo ya Minziro - Mutukula itatengenezwa wananchi wapate huduma na kuinua shughuli za kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kyombo, Mbunge wa Misenyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii nilitembelea. Ni barabara ambayo inafunguliwa upya. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa haikuwa kwenye mtandao, kwa hiyo, inaweza isionekane, lakini azma ya Serikali ni kuifungua na kuijenga hii barabara. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Mgakorongo kwenda mpaka Mrongo ni barabara muhimu ya kiuchumi kwa Mkoa wa Kagera lakini pia inaunganisha nchi jirani ya Uganda. Barabara hii ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni barabara kuu inayounganisha Tanzania na Uganda kupitia mpaka wa Murongo ambayo inaanzia Umugakarongo - Kigarama hadi Murongo.

Mheshimiwa Spika, tunavyoongea sasa hivi, taratibu za manunuzi zinaendelea na ikiwezekana barabara hii itatangazwa kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Utegi – Kowaki – Kinesi ni barabara iliyoahidiwa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli toka akiwa Waziri wa Ujenzi. Nataka nijue ni lini sasa utekelezaji wa ujenzi wa lami wa barabara hii kutoka Kowaki mpaka Kinesi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii iliahidiwa na kiongozi. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeratibu ahadi zote ikiwepo na hii barabara ambayo ameianisha. Nimhakikishie kwamba barabara hii itajengwa kadri Serikali itakapopata fedha. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Barabara ya Guguni inaanzia Tengeru Sokoni hadi Mererani, inaunganisha mikoa miwili ya Arusha na Manyara.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo Mbunge wa Meru, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri barabara hii naifahamu, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye mpango wa kujenga kwa kiwango cha lami na tukizingatia inakwenda kwenye migodi yetu kule Tanzanite. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ukurasa 177, ipo barabara ya kutoka Same – Mkomazi - Umba Junction - Maramba hadi Tanga.

Je, ni lini upembuzi yakinifu na usanifu wa kina utafanyika kwa barabara hii kuunganisha Mkoa wa Kilimanjaro na Tanga kupitia Wilaya ya Lushoto na Mkinga? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Je, ni lini Serikali sasa itakamilisha upembuzi wa kina na usanifu katika kipande cha kutoka Mlalo kwenda Umba Junction kuungana na barabara hii ambayo nimeishaitaja? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Same - Kisiwani kuja Mkomazi ilikuwa inajengwa kwa vipande. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge wa Mkoa wa Kilimanjaro hasa Mheshimiwa Mama Anna Kilango ambaye inamhusu sana barabara hii, kwamba barabara hii ambayo ina urefu usiopungua kilometa 92 inatangazwa yote kujengwa kwa kiwango cha lami na ipo kwenye hatua mbalimbali za kutangaza zabuni.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa swali lake la pili, kuhusu barabara hii ya Mlalo - Umba Junction Serikali inaanza upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Serikali hutumia fedha nyingi sana katika kutengeneza barabara, lakini barabara hizo kwa muda mfupi tu huwa zinamomonyona na kuota manyasi: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutenga fedha kwa ajili ya maintance ya barabara hizi ili kuzinusuru? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kamguna kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara nyingi ambazo ni za changarawe ama za vumbi ni kweli kwamba hazidumu kwa muda mrefu na ndiyo maana zinatengewa fedha kwa ajili ya matengenezo ya kila mwaka. Azma ya Serikali ni kujenga barabara zote kwa kiwango cha lami, lakini barabara hizi ni gharama, kwa hiyo, inategemea na upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, zile barabara kubwa za mkakati ndiyo tutaanza kuzijenga kwa lami, lakini kadri bajeti itakavyoruhusu, mpango ni kuzijenga barabara zote kwa lami zikiwepo na barabara za Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii. Mkoa wa Tanga haujaunganishwa na Mkoa wa Manyara pamoja na Mkoa wa Morogoro kwa barabara ya lami. Ni lini Serikali itajenga barabara Handeni – Kibilashi – Kiteto – Kondoa - Singida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niseme Serikali imepokea ushauri ulioutoa. Nikuhakikishie kwamba katika bajeti ijayo limezingatiwa na tutaendelea kuzingatia zaidi ili kuokoa hizi barabara ambazo tayari zimeshajengwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Reuben Kwagilwa Mbunge, nataka nikuhakikishie kwamba barabara hii ambayo tumeitaja kutoka Handeni - Kiberashi kwenda Kibaya ni barabara ya changarawe na tayari tupo kwenye hatua za manunuzi, kilometa 50 kuanzia Handeni kuja Kiberashi kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami; na kama taratibu zote zitakamilika, barabara hii itaanza kujengwa mwaka huu wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Nataka kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, barabara ambayo inaanzia Dumila kupita Turiani kupita Kata ya Negelo hadi Vibaoni Handeni, ni barabara muhimu sana. Kwa upande wa Morogoro imeshakamilika kwa kiwango cha lami: Je, ni lini kilometa 120 kwa kiwango cha lami itakamilishwa?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Omari Kigua, Mbunge wa Kilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoiainisha imeshafanyiwa usanifu; na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kwa umuhimu wa barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, hapo ni upatikanaji wa fedha tu, once tutakavyopata barabara hii itaanza kujengwa. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Mkoa wa Tabora hadi leo haujaunganishwa na Mkoa wa Mbeya na Mkoa wa Songwe; na kipande muhimu kabisa ambacho kinaunganisha mikoa mitano ni kipande cha kutoka Ipole mpaka Rungwa ambacho usanifu wa kina ulikamilika na tayari shilingi bilioni tano zikatengwa mwaka huu.

Ni lini hiyo barabara itajengwa ili Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Mbeya na Songwe ziunganishwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kipaumbele ni kuunganisha mikoa na mikoa na barabara aliyoitaja siyo tu kwamba ni mkoa, lakini pia ni kati ya zile barabara kuu kutoka Tabora - Ipole hadi Rungwa ambayo inaunganisha na barabara inayotoka Manyoni - Singida kwenda Makongorosi.

Mheshimiwa Spika, kipande cha Manyoni - Itigi kuja Rungwa tunategemea muda wowote kutangazwa; na kipande cha Ipole kuja Rungwa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami ili barabara hiyo ambayo inaunganisha siyo tu na Tabora, ila na mikoa mingi ya Kaskazini iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Bariri kwenda Hunyali na kwenda mpaka Mgeta ni barabara ambayo iko kwenye barabara inayotoka Mwanza kwenda Musoma na barabara inayokwenda Serengeti. Kipande hicho cha barabara Mheshimiwa Rais Samia alipokuwa Bunda tuliomba kwamba kipande hiki kijengwe kwa kiwango cha lami. Ni lini barabara hii itajengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa hii ni ahadi ya Rais, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara inaendelea kuifanyia kazi ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kama Mheshimiwa alivyokuwa ameahidi. Kwa sababu hayo sisi kwetu ni maelekezo na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutatekeleza kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kuhusu ujenzi wa barabara ya kutoka Maramba kwenda Humba kwenda Mlalo. Ni ipi kauli ya Serikali juu ya kipande cha kuunganisha kutoka Maramba - Mashewa kwenda Old Korogwe mpaka Korogwe Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoainisha ipo kwenye mpango wa kukamilisha usanifu wa kina wa barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge inayoanzia Old Korogwe hadi Mabokweni kama nimemwelewa. Nadhani ndiyo hiyo barabara; ipo kwenye ukamilishaji wa kufanya usanifu ili iweze kuanza kwa kiwango cha lami baada ya kukamilisha usanifu. Ahsante.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara ya kutoka Masasi - Nachingwea kwenda Liwale ni barabara ya mkakati: Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja inaanzia Mtwara - Mnivata - Newala hadi Masasi, ina urefu wa kilometa 210. Kilometa 50 atakubaliana nami zimeshajengwa; na tunavyoongea sasa hivi, tupo kwenye hatua za mwisho, African Development Bank wanaijenga hiyo barabara; na kuanzia mwezi Tisa ama wa Kumi hii barabara itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami kilometa zote 160. Ahsante.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na nia nzuri ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inayoongozwa na Rais wetu mpendwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na wingi wa abiria wanaotumia uwanja wa ndege wa Bukoba na kutokana na ufinyu na huduma hafifu za uwanja wa ndege wa Bukoba. Uwanja wa Bukoba mwaka 2020 tulipokea abiria zaidi ya 44,000 na mwaka 2021 tumepokea abiria 45,000.

Je, Serikali haioni kuna uharaka wa kujenga Uwanja wa Ndege wa Omukajunguti?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika majibu ya Serikali imesema wamefanya tathmini ya kulipa watu watakaopisha ujenzi wa uwanja huo.

Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa wakazi wa eneo lile wa Mkajunguti ili waweze kupisha ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Omukajunguti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na idadi kubwa ya abiria ambao ndio wanatumia uwanja wa Bukoba ndiyo maana Serikali imeamua kwamba kuna haja ya kujenga uwanja mkubwa zaidi kwa sababu uwanja wa Bukoba kwa mahali ulipo hauwezi kuendelezwa kwa maana ya kuipanua na ndio maana Serikali imetafuta eneo jipya ambalo uwanja mkubwa unaweza kujengwa ili kuruhusu ndege kubwa hasa tukizingatia umuhimu wa uwanja huo na abiria walivyo wengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la fidia, Serikali ilishafanya tathmini ya awali ambayo kwa mujibu wa fidia hatuwezi kuitumia tulifanya tathimini ilikuwa inaenda kwenye bilioni tisa. Kwa hiyo, kuna utaratibu tunaufanya tuweze kurudia ile tathmini twende na hali ya sasa na mara tutakapokamilisha basi fidia italipwa kabla ya kuanza ujenzi wa uwanja huo wa ndege wa Omkajunguti. Ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru; kwenye Wizara hiyo hiyo ya Ujenzi na Uchukuzi tuna changamoto kubwa sana ya barabara ya Mafinga – Mgololo na Nyororo – Mtangwo ambazo zimeahidiwa kuanzia Serikali Awamu ya Nne mpaka Awamu ya Tano, na tarehe 26 Aprili, 2021 Serikali Awamu ya Sita imetoa commitment letter kuanza kujenga barabara hizo.

Nataka kujua ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa ahadi hii ya kuwajengea barabara wananchi Mufindi Kusini ili waweze kunufaika na barabara hizo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliamuahidi Mheshimiwa Mbunge na ni ahadi ya viongozi wa Kitaifa tangu Awamu ya Kwanza kwamba barabara hii ambayo ni barabara kuu lakini ni barabara kimkakati kwamba tutaijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge endapo bajeti ambayo tunaenda kuipitisha itapitishwa bila mabadiliko, barabara hii imeweza kuwekwa kwenye mpango ili iweze kujengwa kwa kiwango lami hasa tukizingatia kwamba sehemu kubwa ya mazao ya mbao tunayoyaona Tanzania yanatoka katika eneo hilo.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naomba niende moja kwa moja kwenye swali langu dogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na uwepo wa viwanja vya ndege gharama au nauli za ndege zimekuwa juu sana nini kauliya Serikali kuhusiana na kuhakikisha nauli hizi zinakuwa himilivu kwa Watanzania hasa baada ya kuwa wamehamasika sana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la nauli ni suala la kibiashara na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wenzetu wa ATCL kuna taratibu ukifanya booking mapema bei inashuka lakini kama utanunua tiketi utaratibu wa mashirika mengi ya ndege kama utachelewa kununua tiketi ya ndege siku zote bei inakuwa juu, lakini kama utafanya booking mapema basi nauli inakuwa ni ya chini.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kuuliza Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inakamilisha uwanja wa ndege wa Songwe kwa kuweka vifaa vya kupoozea mazao yaani cold rooms ili kusudi wananchi wa Wilaya ya Mbozi na mikoa ya Nyanda za Juu Kusini waweze kuhakikisha kwamba wanasafirisha maparachichi na matunda mengine?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hasunga, Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, uwanja wa ndege wa Songwe sasa hivi tuko kwenye kukamilisha kuufanya kuwa kati ya viwanja vikubwa vya Tanzania vya ndege ambapo kutakuwa na uwezo wa kupokea ndege zote kubwa zinazoruka katika Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hatua ya pili ni kujenga storage facility zikiwepo na hizo za kutunza vifaa ambavyo ni baridi kwa ajili ya kusafirisha nje na ndio maana Serikali ina mpango tayari wa kununua ndege ya kusafirisha mizigo. Kitu cha kufanya ni kujenga hizo storage facility ikiwepo Mkoa wa Mbeya, ahsante.
MHE. ROBERT C. MABOTO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, barabara ya Buramba – Bunda - Nyamuswa inayotekelezwa kwa kiwango cha lami wananchi wamebomolewa nyumba zao pale. Ni lini Serikali itawalipa fidia yao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maboto Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ilishafanyika, wananchi walishaainishwa na sasa hivi Serikali inafanya kupitia yale malipo ili waweze kulipa fidia hiyo.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, licha ya juhudu za Serikali za kuendelea kukarabati viwanja wa ndege bado vingi vimekuwa vinafanya kazi mchana tu. Nini mkakati wa Serikali kuhakikisha viwanja vinafanya kazi saa 24?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi viwanja vyote tunapoongelea kiwanja cha Mbeya, kiwanja cha Songwe, kiwanja cha Mtwara, kiwanja cha Msalato, kiwanja cha Geita na hata hivyo viwanja vile tunavyojenga Sumbawanga, Kigoma, Tabora na Shinyanga vyote viko kwenye mpango wa kujengewa taa ili viweze kufanya kazi saa 24 na kazi hiyo inaendelea. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli majibu ya Naibu Waziri yananifikirisha sana. Mfadhili ameshapatikana, fedha zimeshatolewa, mkataba umesainiwa mwaka 2017 na wameomba price adjustment. (Makofi)

Je, ni lini Serikali itaongeza hizo fedha ili kazi ianze?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili Naibu Waziri amesema kwamba ujenzi utaanza endapo mkandarasi atawasilisha hati ya dhamana ya malipo; ni nini kauli ya Serikali endapo mkandarasi hatawasilisha kwa wakati kama alivyosema kwenye jibu lake la msingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, price adjustment haizuii uwanja kuanza, lakini ni utaratibu kwa kuwa mkataba ulikuwa wa zamani lazima tuwajulishe hawa wafadhili kwamba kutakuwa na ongezeko la bei na endapo pia hawatataka kuongeza Serikali itaendelea kujenga huu uwanja kwa ile nyongeza ambayo itakuwepo kwani tayari wameshatoa milioni 12 United States dollars kwa ajili ya kuanza ujenzi wa viwanja hivyo.

Mheshimiwa Naibu spika, na hati ya dhamana ni kwamba tayari mkandarasi yuko tayari kuanza kujenga na sasa hivi anachofanya tu ni kuandaa hizo hati ili aweze kuziwasilisha baada ya hiyo fedha kutolewa na wafadhili, ahsante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana ni Asia Halamga, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Naibu Waziri amewahi kuja kukagua eneo la ujenzi wa uwanja wa ndege lililopo kata ya Mwada eneo lenye takribani ya hekari 600 na halina mgogoro wowote.

Je, ni lini Serikali sasa italeta fedha kwa ajili ya ujenzi wa uwanja wa ndege wa Mkoa wa Manyara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli uwanja huu utajengwa eneo linaloitwa Mwaga na sasa hivi tunavyoendelea ni kwamba tuko kwenye hatua ya utwaaji wa eneo hilo na pia lilikuwa ni agizo la Mheshimiwa Makamu wa Rais wakati anafungua daraja la Magala kwamba kazi hiyo ifanyike haraka. Kwa hiyo Serikali tuko tunaendelea kulifanyia kazi tuweze kutoa na kuwalipa fidia halafu ujenzi uanze.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa nafasi ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge hili kwa bajeti inayoendelea inayoishia Juni, 2022, ilipitisha kwamba kiwanja cha ndege cha Kilwa Masoko kifanyiwe ukarabati na maboresho, mpaka tunazungumza kazi iliyofanyika ni ya kilometa moja kwa kiwango cha changarawe bado mita 950.

Nini maelezo ya Serikali kuhusiana na mita 950 zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge Mbunge wa Kilwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali ilivyoahidi tumeshakamilisha kilometa moja na tutaendelea kuzikamilisha hizo kilomita 900 zilizobaki kwa kiwango cha changarawe ili tuweze kutimiza ile ahadi ambayo tuliahidi kuifanya, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kigoma ni lango kuu la uchumi wa nchi yetu kwa sababu umepakana na nchi za jirani za DRC Congo na Burundi. Mara nyingi serikaliimekuwa ikiahidi kuja kujenga uwanja wa ndege Kigoma na kuweka taa kwa maaa ya ndege ziweze kuruka usiku.

Sasa nataka Waziri aniambie ni lini Serikali itakuja kuweka taa na kuongeza uwanja wa ndege wa Mkoa wa Kigoma kwa sababu Kigoma imepakana na nchi jirani za Congo na Burundi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kigoma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kiwanja cha Kigoma ni kati ya viwanja vinne ambavyo ni Kigoma, Tabora, Sumbawanga na Shinyanga ambavyo vinafadhiliwa na European Investment Bank na ni kati ya viwanja ambavyo tayari fedha imeshatolewa na moja ya kazi ambayo fedha hii inaenda kufanya ni kujenga uzio, jengo la abiria, runway ikiwa ni pamoja na kuweka taa ili kiwanja hiki kiweze kufanya kazi saa 24.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tayari Serikali inaenda kujenga huu uwanja kama ulivyosema. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante uwanja wa ndege Mkoa wa Njombe haupo kabisa kwenye utekelezaji wa bajeti uliopita na hata bajeti iliyopo ya sasa, lakini kwenye ilani umekuwa ukiutaja kama ni moja kati ya viwanja mnaenda kuvitenga.

Wananjombe wanauliza ni upi mkakati wa Serikali kujenga uwanja wa ndege Mkoa wa Njombe kwa sababu uwekezaji wa parachichi na mambo mengine sasa hivi wanauhitaji mkubwa, lakini wananjombe walioko nje wengi matajiri wanahitaji kusafiri kupitia ndege kurudi Njombe ni upi mkakati wa Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nikweli kwamba uwanja wa Njombe ni muhimu na eneo lipo tayari. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itakapopata fedha na hasa kulingana na umuhimu wa uwanja huo tutaanza kufanya kwanza utwaaji na kulipa fidia lakini pia kuanza usanifu wa kina, lakini hili Mheshimiwa Mbunge itategemea na upatikanaji wa fedha na utekelezaji wa ilani ni wa miaka mitano. Kwa hiyo nikuhakikishie kwamba hata kama kwa sasa hatujaanza kutekeleza lakini utatekelezwa katika miaka hii mitano, ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida uko karibu sana na Makao Makuu ya nchi Dodoma na kwa sababu ya kiusalama uwanja wa ndege wa Singida ni muhimu sana na kwa sababu Marais wote wawili wametaja kwenye hotuba zao hapa Bungeni Rais John Pombe Magufuli pamoja na Rais Samia Suluhu Hassan walisema katika viwanja 11 na kiwanja cha Singida kitajengwa.

Sasa naomba nijue ni lini sasa Serikali itatenga fedha ili kujenga uwanja ule ambao upo karibu na Makao Makuu ya nchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, maelezo ya Mheshimiwa Mbunge ni sahihi na ni kweli kwamba viongozi wameahidi uwanja huu uweze kujengwa na mimi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara tayari ina mpango wa kuanza kufanya tathmini ya uwanja huu ili iweze kuujenga lakini pia kama ulivyosema ni uwanja ambao upo karibu na Dodoma kwa ajili ya usalama. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo Wizara inalo na muda si mrefu itaanza kulifanyia kazi, ahsante.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuuliza ni lini uwanja wa Mbeya utaanza kutumika usiku na mchana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Mlaghila Jumbe, Mbunge wa Kyela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi tunavyoongea uwekaji wa taa kwa uwanja wa Mbeya ambao ni Songwe airport upo pengine kwenye asilimia 95 uwekaji wa taa, runway imeshakamilika zaidi ya mita 3000, uzio na sasa hivi tunakamilisha pia jengo la kisasa la abiria. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba uwanja huu utaanza kutumika, taa zimeshajengwa na utaanza kupokea ndege usiku na mchana ili kuhakikisha kwamba uwanja huo unatumika kwa asilimia 100, ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa kwa mara ya saba kulalamikia uwanja wa Sumbawanga Mjini, leo nataka commitment ya Serikali, ni lini kazi ya ujenzi wa uwanja wa Sumbawanga Mjini utaanza?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Serikali sasa ina mpango gani wa kuweka basi hata route ya kutoka Songwe moja kwa moja mpaka Dodoma wakati huo inaendelea kujipanga kwa ujenzi wa Sumbawanga Mjini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Rukwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, ilitakiwa kiwanja hiki kianze kujengwa mwaka wa fedha wa 2017/2018, lakini kutokana na changamoto ambayo ilikuwepo EIB hawakutoa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Mbunge amenisikiliza tayari EIB wameshatoa Dola Milioni 12 kwa ajili ya kuanza viwanja hivi vinne. Lakini kwa kuwa usanifu ulifanyika zamani, Mkandarasi ameomba mkataba huo urudiwe kwa sababu ya gharama, na kwa sababu gharama zitabadilika lazima tuwasiliane na mtoa fedha ili aweze kutoa no objection.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu langu nimesema kama atatoa kwa sababu Mkandarasi yupo basi itaanza kujengwa kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu route ya Songwe hadi Dodoma, tumelichukua lakini pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Shirika letu la Ndege la ATCL inayafanyia kazi masuala yote haya ya usafiri kuona namna ya kuunganisha kati ya Dodoma - Mwanza, Dodoma- Kilimanjaro, Dodoma – Mbeya, lakini hii itategemea na wao watakavyofanya study kuona kama wakifanya hivyo kwao biashara itakuwa ni nzuri. Kwa hiyo, wapo wanaendelea kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Kwa kuwa hii ni Wizara ya Ujenzi, Je, Mheshimiwa Naibu Waziri ni lini TANROAD wataenda kutengeneza barabara ambayo wameiparua pale Kata ya Segerea kwa muda wa Miezi Mitatu sasa na wananchi wanapata vumbi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Kalua Mbunge wa Segerea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hii barabara imekuwa inatengenezwa kwa vipande na kipande anachokisema kweli tulikuwa tumeanza kufanya maandalizi lakini kulikuwa na shida ya kupata msamaha wa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba msamaha huu umeshatolewa na mara moja Mkandarasi atakuwa yuko site kuondoa lile vumbi ambalo linaleta shida kwa wananchi wa Jimbo la Segerea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tu kupitia nafasi hii pia nimjulishe ama kumuagiza Meneja wa TANROADS kwamba kwa kuwa msamaha umeshatolewa basi Mkandarasi aende site ili aweze kukamilisha kazi ambayo anatakiwa aifanye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, uwanja wa ndege wa Ruganzo umejengwa muda mrefu umechoka na sasa unahitaji ukarabati. Na kwa kuwa, sasa Ngara imefunguka, wageni ni wengi, Nickel inatakiwa kuchimbwa na biashara mpakani imeshamiri.

Je, ni lini Serikali itakuja kukarabati uwanja wa ndege wa Ruganzo?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndaisaba, Mbunge wa Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala lake limepokelewa na tunajua wageni wengi wanaenda Ngara ambapo ni mbali kutoka viwanja vyote vya ndege ambavyo viko karibu. Kwa hiyo, suala lake tumelichukua na Serikali itatafuta fedha ili kuweza kukikarabati kiwanja hiki ili wageni na watu mbalimbali waweze kufika kwa urahisi kwa ndege katika Wilaya ya Ngara.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Naibu Waziri anajibu swali la msingi, alitaja viwanja Vinne lakini kwa bahati mbaya kiwanja cha Tanga sijakiona ilihali Tanga tuna ujenzi wa bomba la mafuta na ujenzi huu utahitaji uwanja wa ndege wa Tanga uwe umepanuliwa kwa ajili ya kutoa huduma.

Je, ni upi mkakati wa Serikali kupanua uwanja wa ndege wa Tanga ili kuruhusu shughuli za bomba la mafuta?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanja nilivyovitaja vine vipo kwenye package moja, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Shangazi kwamba Serikali kama bajeti ya mwaka huu tunaokwenda kuipitisha itapita, kuna viwanja vingine ambavyo pia tuna mpango wa kuvipanua na hasa kiwanja alichokisema cha Tanga ambacho katika kipindi hiki ni kiwanja muhimu sana kwa shughuli ambazo zinaendelea katika Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuna uwanja wa Tanza, kuna uwanja wa Lake Manyara, Simiyu, Lindi, ni kati ya viwanja ambavyo tunategemea kama bajeti itapita, vitakuwa ni baadhi ya viwanja ambavyo tutavipanua na kuvifanyia maboresho makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, ujenzi wa uwanja wa ndege wa Mkoa wa Simiyu upo kwenye Ilani na eneo tayari limeshajengwa.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa ndege katika Mkoa wa Simiyu?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyomjibu Mheshimiwa Shangazi, nimetaja kiwanja cha Simiyu kwamba ni kati ya viwanja ambavyo vipo katika bajeti ambayo tunaenda kwenye mpango wa kuanza kivijenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uwanja wa Njombe Mjini ni uwanja ambao wananchi wanauhitaji mkubwa sana wa usafiri wa anga, na kwenye ahadi ya Chama cha Mapinduzi umesemwa, Waziri Mkuu ameahidi.

Je, ni lini sasa uwanja huo utaanza ujenzi?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli uwanja wa Njombe unatakiwa ujengwe na tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika. Serikali inatafuta fedha ili iweze kufanya usanifu wa kina wa uwanja huu ili uweze kujengwa hasa tukizingatia kwamba nguvu kubwa ya kiuchumi ya Mkoa wa Njombe, kwamba tunahitaji kuwa na uwanja kwa ajili ya ku-attract si tu wafanyabiashara, lakini pia tunajua ndiyo kuna uwekezaji mkubwa wa madini ya makaa ya mawe na chuma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuna uhakika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha kufanya usanifu na hatimae kuujenga huo uwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali madogo ya nyongeza. Kwanza naipongeza Serikali kwa hatua hiyo, sasa tunaelekea kwenye upembuzi yakinifu pamoja na usanifu. Sasa hamu ya wana Manyara ni kuwa na kiwanja cha ndege. Sasa Serikali imejipangaje kukamilisha hatua hiyo ya usanifu?

Swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani sasa wa kufidia wananchi ambao maeneo yao yatatwaliwa kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha ndege baada ya kukamilisha uthamini huo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaanza, kama nilivyosema, tumeshatafuta mhandisi elekezi kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina; na huyo ndie atakayetupa sasa gharama halisi ya fidia. Baada ya hapo Serikali basi itatafuta fedha ili kabla hatujaanza ujenzi tuwafidie hao wananchi amabo watapisha ujenzi wa eneo hilo, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Wizara ya Ujenzi na majibu yenye faraja kwa wakazi wa Kigamboni hususan maeneo ya Mwasonga, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Wizara ya Ujenzi kupitia TANROADS ilifanya ujenzi wa kipande kidogo cha kilometa moja kutoka Kibada junction kwenda Mwasonga. Sasa hivi ni zaidi ya mwaka mmoja na nusu, kipande kile cha kilometa moja hakijakamilika.

Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi wa kile kipande cha kilometa moja ambao ujenzi wake umeanza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; barabara nyingi pale Kigamboni zimemeguka kutokana na kukosa kingo kutokana na magari mazito kuchepuka nje ya barabara na kwingine barabara zimekatwa kashata kutokana na ubovu lakini hazijakarabatiwa. Sasa ni lini barabara zile zitakarabatiwa lakini vile vile kuwekwa kingo ili barabara zile zisiendelee kumomonyoka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Faustine Engelbert Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mkandarasi ambaye alipewa kazi ya kukamilisha kipande cha kilometa moja amechelewa na tayari ameshaandikiwa barua na anatumikia adhabu ya liquidated damage na kama atakuwa hajakamilisha ndani ya siku 100, tunafunga mkataba kumtafuta mkandarasi mwingine. Hivi tunavyoongea yupo anakamilisha hiyo kazi na yuko kwenye 75%-80%.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu mashimo na kingo za barabara, tayari tumesham-engage mkandarasi, Mark Construction na ameshaanza kazi na kuharibika kwa barabara hii ni kweli ni barabara ya zamani, traffic imeongezeka sana na magari mengi makubwa yanapita. Kwa hiyo tayari mkandarasi yupo kwa ajili ya kukarabati barabara hizo za lami. Pia hata hizo za changarawe tumeshamweka mkandarasi kuhakikisha kwamba anakarabati hizo barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni lini Barabara ya Masasi – Nachingwea - Liwale itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tecla Ungele, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja sasa hivi zinafanyiwa evaluation, ndiyo moja ya barabara ambazo ziko kwenye EPC+F. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa Barabara ya Mbalizi - Shigamba ni ahadi ya muda mrefu ya viongozi wetu na pia ni kiungo muhimu kwa Tanzania na Malawi. Je, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunavyoongea sasa hivi, Mhandisi Mshauri yuko site akifanya usanifu wa kina na baada ya hapo, barabara hii itatafutiwa fedha kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya Karatu – Njiapanda - Mang’ola - Lalago kwa kiwango cha lami. Je, ni lini ahadi hii itatekelezwa ili barabara hiyo ijengwe kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ahadi hiyo ipo ya kujenga hiyo barabara ya Karatu hadi Lalago kwa kiwango cha lami. Serikali bado haijaufuta mpango huo, inaendelea kutafuta fedha na fedha zikipatikana basi barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nataka kujua ni lini Barabara ya Nyakanga kwenda Nyaishozi kuja mpaka Benako itajengwa kwa kiwango cha lami, kwa sababu ni barabara kuu inaunganisha Tanzania na Rwanda?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tumeshaanza kuijenga kwa kiwango cha lami kilometa 60 na barabara iliyobaki, African Development Bank wako kwenye majadiliano ili kuikamilisha yote kuunganisha Tanzania, Burundi na Rwanda.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Barabara ya Dar es Salaam inaunganisha baina ya Dar es Salaam na Pwani. Vilevile barabara hizi ni kiunganishi kati ya Mkuranga na Ilala ambayo ni Kiguza – Hoyoyo – Mwanadilatu - Msongola. Sasa lini barabara hizi zitajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hizi ni muhimu kama alivyozitaja na zinaunganisha barabara kuu na barabara hizi ambazo tunasema ni feeder roads. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kufanya usanifu wa kina na baadaye ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Kiranjeranje - Makangaga – Nakiu - Nanjilinji na hatimaye Ruangwa imefikia hatua gani ili ijengwe kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii imeshafanyiwa usanifu na Serikali inatafuta fedha kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Kiranjeranje hadi Ruangwa, ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itajenga Barabara ya Mogitu - Hydom kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, barabara aliyotaja Mheshimiwa Hhayuma, ni link kati ya Barabara ya Babati - Hydom kwenda Sibiti. Kwa hiyo itakavyoanza kujengwa, hicho kipande kitakuwa ni sehemu ya hiyo barabara.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali, barabara ya kutoka Chimara kwa maana ya Mfumbi kuelekea Matamba-Kitulo, kilometa 51. Barabara ambayo inaelekea kwenye hifadhi ya utalii. Ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa sababu upembuzi yakinifu ulishaanza kufanyika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuifungua barabara hii kwa ajili ya kuunganisha maeneo ya Chimara - Itamba hadi Makete, lakini pia tunajua tutakuwa tunafungua utalii eneo hilo, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa barabara ya kutoka Mtwara mpaka Msimbati, ambayo takribani sasa ina zaidi ya miaka 15, barabara hii inajengwa kwa vipande vipande? Sasa hivi wamejenga kilometa tano tu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtenga, Mbunge wa Mtwara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tunajenga kwa awamu kadiri fedha inavyopatikana. Azma ya Serikali ni kujenga barabara yote. Kwa hiyo Serikali inatafuta fedha ili zikikamilika basi tuweze kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza kufanya upembuzi yakinifu Barabara ya kutoka Nyoni hadi Mipotopoto-Mitomoni kwa ajili ya ujenzi wa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo kwenye ilani hii barabara kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami na tunategemea katika bajeti ijayo iweze kuingia ili iweze kufanyiwa usanifu wa kina ikiwa ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Niishukuru sana Serikali kwa mpango iliyoweka, tuiombe sasa tu zabuni iwahi na mkandarasi apatikane ili wanachi wanufaike na taa hizi za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina swali moja tu la nyongeza mahali hapa. Ni nini sasa Mkakati wa Serikali ya uwekaji wa taa za barabarani kwenye miji iliyoendelea ikiwemo Magu, Busega pale Masanza pamoja na Nasa Ginnery lakini pamoja na Itilima Mkoani Simiyu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nitoe tu maelezo kwa ajili ya swali hili. Kwamba kwa sasa Serikali imetoa mamlaka kwa Mameneja wa Mikoa wote wa TANROADS kupitia mikutano ya mifuko ya barabara pamoja na RCC kuanisha miji yote mikubwa ambayo imekua na inahitaji taa ili waweze kuziombea hela kwa ajili ya kuweka barabara kwenye miji yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa sasa kwa barabara zote ambazo zinajengwa kwa sasa imekuwa ni sehemu ambapo tunapoanza kujenga barabara miji yote inawekewa taa. Kwa hiyo inakuwa ni sehemu ya gharama ya zile barabara. Kwa hiyo ni pamoja na hiyo miji aliyoisema Mheshimiwa Simon Songe, ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi lakini pia namshukuru Rais wa Jamhuri wa Tanzania alipofanya ziara katika Jimbo langu la Rungwe aliahidi kuweka taa katika Mji Kiwila, Mji mdogo wa Tukuyu pamoja na Ushirika.

Je, ni lini sasa taa hizo zitawekwa katika miji hiyo ambayo nimeitaja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantona, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyoongea miji ya Kiwila, Tukuyu na Ushirika itawekewa taa; na sasa hivi Mkandarasi ameshapatikana, wako kwenye hatua za mobilization, ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kunapokuwa na taa za barabarani kwanza kuna kuwa na usalama wa wasafiri lakini vile vile wananchi wanafanya shughuli zao za uchumi mpaka usiku kwa sababu kuna usalama.

Je, ni lini Miji ya Hedaru, Makanya, Mji mdogo wa Same, Njoro Kisiwani pamoja na Mwembe watawekewa taa za barabarani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Mathayo David, Mbunge wa Same, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, miji aliyoitaja, Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro ameshawasilisha maombi na tunategemea fedha itaenda mwaka huu ili miji hiyo iweze kuwekewa taa kwa ajili ya usalama lakini pia na kupendeza miji aliyoitaja, ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa tarehe 22 Mwezi wa Nane 2022 Serikali ya kuanza kujenga Barabara ya Morogoro – Njombe boarder kwa kiwango cha kilometa 100 kutoka Ifakara kwenda Chita.

Je, Wananchi wa Mlimba wangependa kujua taa inaweza kuwa component kwenye tenda hasa kwenye maeneo ya miji kama Mchombe na Mgeta na Mlimba Mjini? Ahsa nte.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunambi, Mbunge wa Mlimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwa sasa barabara zote ambazo tunazi – design na kuzijenga, miji yote ambayo inapitiwa na hiyo barabara inawekewa taa. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Mlimba, kwamba miji yote ambayo itapitiwa na hiyo barabara kilometa 100 taa itakuwa ni sehemu ya hiyo kandarasi, ahsante.
MHE. HAJI MAKAME MLENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuweza kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini pia naomba kuuliza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa baadhi ya viwanda au baadhi ya wadau mbalimbali hutengeneza bustani nzuri tu kandokando ya barabara, lakini hulipishwa fedha nyingi na Wizara yako.

Je, huoni sasa ni muda muafaka wa kuondoa tozo hizo ili wadau hao waendelee kutengeneza bustani nzuri hasa katika maeneo ya majiji yetu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Wizara yako ina mkakati gani wa kuwatia moyo wale wote wanaotengeneza bustani nzuri kando kando ya majiji badala ya kuwalipisha fedha nyingi pale wanapofanya hivyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Haji Makame Mlenge, Mbunge wa Chwaka kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tuna kitu kinachoitwa road maintenance manual ambacho ni kama mwongozo wa watu wote ambao wanaomba kutumia hifadhi ya barabara na kule ndiyo tumetaja gharama ya kila shughuli ambayo mtu anaifanya ikiwepo ni pamoja na kuweka bustani kando kando ya barabara.

Kwa hiyo, tuna mwongozo ambao upo, lakini kama bei ni kubwa, tutalichukua na kuliangalia kama limekuwa ni changamoto kwa watu ambao wanatumia eneo la kandokando ya barabara kwa ajili ya kutunza mazingira na kupendezesha mji.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la pili kama alivyosema, sisi tuko tayari kukaa na hao watu ili tuwatie moyo na bado nafasi huwa zinatangazwa, yaani kwamba barabara ikishajengwa unaruhusiwa kwenda kuomba na kupewa kibali cha kuweka shughuli ambazo siyo za kudumu kandokando ya barabara ikiwa ni kutunza mazingira na kupendezesha miji, na kwa miji tunashirikiana sisi na wenzetu wa TAMISEMI ambao wana barabara nyingi katika miji, majiji na manispaa, ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Spika, uchafuzi wa mazingira kwenye nchi yetu ni jambo ambalo linaendelea kushamiri sana, kwa mfano unaweza wakati unatoka Dar es Salaam labda kuelekea Momba, ukapita sehemu kabisa hakuna makazi ya watu, lakini utakuta takataka nyingi sana zimejaa barabarani.

Je, Serikali haioni kuchukua ushauri huu kutumia vijana wetu ambao wako mtaani hawajapata ajira waliomaliza ngazi za certificate, diploma na hususan wale ambao wamepitia na jeshini hawajapata ajira. Je, hamuoni muanzishe programu maalum kwa ajili vijana hawa kutunza mazingira yetu ikiwa ni pamoja na kuweka faini kwa mtu yeyote ambaye atabainika anatupa takataka hovyo ili kipato pia cha kuwalipa vijana hawa kitokane na faini ambazo tutakuwa tunatozwa sisi wenyewe Watanzania kwa kutokutunza mazingira yetu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Momba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza siyo utaratibu kwa mtu unaposafiri na kutupa takataka nje. Naomba suala hili niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwa ujumla kwamba siyo outaratibu na ndiyo maana magari mengi ya usafiri sasa hivi kuna utaratibu ambao kunakuwa na dustbin ambayo mtu yeyote msafiri anatakiwa aweke uchafu na mahali tukifika gari basi watakwenda kutupa takataka.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa vijana nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tumeuchukua kusaidiana na wenzetu wanaotunza miji ambao ni TAMISEMI kuona namna wanavyoweza kufanya kunapotokea uchafu mbalimbali kando kando ya barabara zetu.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali langu la kwanza, hili swali nimeliuliza hii ni mara ya tano sasa ndani ya Bunge hili na kila wakati mnasema Serikali kwamba inatafuta fedha.

Sasa nataka nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, je, hizo fedha zinatafutwa miaka yote hii au lini zitapatikana?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa sasa hiyo barabara ina hali mbaya sana kutoka Mlowo mpaka pale Igamba sehemu ya Zerezeta na Mheshimiwa Naibu Waziri umefika umetumiwa picha umeona uhalisia.

Nini kauli ya Serikali kwa wakazi wa Mbozi wanaopata tabu sana kipindi hiki cha masika kwa hiyo barabara ifanyiwe matengenezo ya haraka na kuondolewa vile vifusi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii anayoitaja ni muhimu sana ya kiuchumi na inayounganisha Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Rukwa na ndiko kunakotoa mpunga mwingi sana katika nchi ya Tanzania.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ndiyo maana Serikali kwanza iliona ijenge daraja la Mto Momba kurahisisha usafiri, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba matarajio ya Wizara kwamba tutaweka kwenye mapendekezo ya bajeti barabara hii iweze kuanza kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, ni kweli kati ya Mlowo na Igamba eneo linaloitwa Zerezeta pamekuwa na changamoto na tulishamuagiza Meneja wa Mkoa aweze kuhakikisha kwamba anafanya marekebisho na kuweka changarawe ambazo ni imara ambazo haziwezi kuteleza ili shughuli za kiuchumi kwenye barabara hiyo ziendelee.

Kwa hiyo, nachukua pia nafasi hii kupitia Bunge kumuagiza Meneja wa Mkoa kuhakikisha kwamba anachukua jitihada za makusudi kuhakikisha kwamba eneo hilo la Mlowo - Igamba eneo la Zerezeta linafanyiwa matengenezo haraka, ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Handeni – Mziha - Turiani hasa ukizingatia kwamba barabara hii ndiyo barabara pekee inayounganisha Mkoa wa Tanga na Morogoro?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tulishaanza kuijenga mpaka Turiani na katika mwaka huu tulitenga kiasi cha Bajeti, lakini barabara hii haikupata kibali cha kuanza kujengwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama alivyosema inaunganisha Mkoa wa Morogoro na Tanga kupitia Handeni, tutaiweka tena kwenye mapendekezo ya bajeti ya mwaka huu ili tuweze kuunganisha Mkoa wa Morogor na Tanga kupitia Turiani - Mziha hadi Handeni.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi; je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara ya Karatu-Endabash-Mbulu kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja tumeshaanza kuijenga kuanzia Mbulu hadi Garbab na tunaendelea. Zabuni ziko zilishafunguliwa zinafanyiwa evaluation kutoka Labay kwenda Hydom. Kwa hiyo tayari tumeshaanza hiyo barabra lakini pia ni barabara ambayo imeingia kwenye mpango wa EPC+F na evaluation zinaendelea.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, ahsante, ni lini utekelezaji wa ujenzi wa barabara ya Kolandoto kwenda Kishapu katika kiwango cha lami utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, barabara hii ipo kwenye mpango wa bajeti kwa ajili ya kuijenga mwaka huu na tutaendelea na mwaka ujao. (Makofi/Kicheko)

MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na kupitisha kwenye mfumo wa EPC katika zile barabara saba, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami barabara ya Mafinga - Mgololo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara tajwa ipo kwenye evaluation, Mgololo - Mafinga.
MHE. JOSEPH L. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, ningependa kufahamu ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa kipande cha barabara kutoka Mawengi mpaka Makao Makuu ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kati ya hicho kipande. (Makofi/Vigelegele)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba tu kwa hekima, Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan amatusaidia sana kutupa fedha kiasi cha shilingi bilioni 7.2 pale Inyala binadamu wengi wamepoteza uhai.

Swali langu naomba kuuliza, je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara ya bypass kuanzia pale Mlima Nyoka mpaka Mbalizi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kipande hicho kiko kwenye sehemu ya Igawa kwenda Tunduma na sasa hivi tupo kwenye evaluation, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM M. NYOKA: Mheshimiwa Spika, je, lini Serikali itajenga barabara ya Mbinga – Mpepai – Mtuha - Lipalamba kwenda Mpepa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina Serikali itatafuta fedha kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, fedha za ujenzi wa barabara ya Mnivata - Newala hadi Masasi imeshapatikana; je, ujenzi utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, evaluation ilishapatikana, wakandarasi wamesha-tender tunasubiri tu barabara hiyo kuanza kujengwa baada ya kupata no objection ya African Development Bank, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika,
lini kipande cha barabara kutoka Kilosa hadi Mikumi kitaanza ujenzi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hiyo aliyoitaja Mheshimiwa ipo inaendelea kuanzia barabara ya Morogoro - Dar es Salaam na tumeshafika Kilosa ikiwa ni mwendelezo wa kwenda Mikumi, ahsante.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, barabara ya Mokongorosi - Rungwa imeahidiwa kwa muda mrefu, je, ni lini Serikali itatoa fedha ili kipande cha Makongorosi kianze kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE: Mheshimiwa Spika, tumeshaanza upande wa Itigi na bajeti itakayofuata tukishapitishiwa tutaanza upande mwingine wa Makongorosi kwenda Itigi, ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imeshatoa takribani shilingi milioni 150 kwa ajili ya upembuzi wa barabara kutoka Kahama - Nyangh’wale – Busisi; je, ni lini upembuzi huo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, tunategemea barabara hiyo ikamilike mwaka huu wa fedha, kwa maana ya usanifu wa kina.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, je, ni lini ujenzi wa barabara ya kutoka Masasi kwenda Nachingwea utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ipo kwenye evaluation kupitia EPC+F. (Makofi)
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Spika, ni lini barabara ya Uru Shimbwe itajengwa kwa kiwango cha lami maana imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, hatua ya kwanza itakuwa ni kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha usanifu wa kina wa barabara husika. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango gani wa kupanua barabara ya kutoka Mpemba mpaka Transfoma Tunduma ili kuepusha changamoto ya mrundikano wa magari ambayo wananchi wamekuwa wakikabiliano nayo ambayo inasababisha ajali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara ya Mpemba kwenda Tunduma ni sehemu ya barabara ya Igawa - Songwe - Tunduma na ipo kwenye evaluation hivi tunavyoongea, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, je ni lini Serikali itaanza rasmi ujenzi wa barabara ya Katumba - Songwe – Kasumuru – Ngana - Ileje?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hiyo ilishatangazwa na tender zimeshafunguliwa, kwa hiyo muda wowote itaanza kujengwa baada ya kumpata mkandarasi, ahsante.
MHE. NG’WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, ni lini ujenzi wa barabara ya kutoka Mwanza Airport kwenda Nyanguge kilometa 46 itaanza rasmi kujengwa kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa katika ilani mbili za uchaguzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara tajwa ni sehemu ya barabara ya bypass, imeshafanyiwa usanifu wa kina na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kujengwa yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itatujengea barabara ya bypass Tunduru Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara husika itajengwa kwa bypass baada ya kufanyika usanifu wa kina. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, je, ni lini barabara ya kutoka Iringa Mjini kupita Kalenga kwenda Kilolo itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, itategemea na upatikanaji wa fedha na tunategemea barabara hiyo muhimu tuiweke kwenye mapendekezo kwa ajili ya kuijenga katika bajeti ambayo tunaiendea sasa hivi.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu ya Naibu Waziri nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kipande cha KM 65 katika barabara hii kutoka Nzega, Itobo mpaka Kagongwa, ndicho kitatumika kubeba mzingo mkubwa wa mabomba ya mradi wa mafuta kutoka Hoima - Uganda mpaka Tanga, kwa hali ilivyo sasa barabara ile ni nyembamba, madaraja madogo haiweze kabisa kubeba mzigo huo mzito wa hayo mabomba ya mradi wa bomba la mafuta.

Mheshimiwa Spika, nilishashauri Wizara ya Ujenzi ikae na Wizara ya Nishati pamoja na wenye mradi EACOP ili waweze kuzungumza namna ambavyo hizi KM 65 kutoka Nzega - Itobo na Kagongwa namna ambavyo wanaweza kuzishughulikia kwa haraka ili mzigo huu mzito uweze kupita.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba Wizara imefikia wapi kukuaa na Wizara ya Nishati na hawa wenye mradi EACOP ili kuzungumzia namna kushughulika na hiki kipande cha KM 65 ili mzigo wa mabomba uweze kupita kwenda kwenye site.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG.GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Zedi, Mbunge wa Bukene kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukuwe nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Zedi kwa jinsi ambavyo amekuwa akifuatilia barabara hii na hasa hiki kipande alichokitaja. Katika eneo alilolitaja ndio kutakuwa na kituo kimoja kikubwa sana kwa ajili ya ujenzi wa bomba la mafuta. Kwa hiyo, anachosema barabara ile haiwezi kuhimili kubeba uzito wa magari yanayopita na ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo sasa inakuwa ni barabara ya Taifa kwa ajili ya uchumi wa Taifa.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inaendelea kuratibu pamoja na wadau wengine ikiwemo Wizara ya Nishati, EACOP na wadau wengine kuhakikisha kwamba tunaijenga hii barabara ili tutakapoanza kazi hii barabara isije ikawa ni kikwazo kwa maana ya madaraja na upana wa barabara yenyewe.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge taratibu zipo zinaendelea. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANTIPAS Z. MGUNGUSI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali lakini barabara hiyo ambayo anaizungumzia kwa sasa kuna dharura kwa maana ya mawasiliano yamekatika baina ya Malinyi na Morogoro Mjini.

Je, Wizara iko tayari kuiongezea TANROADS Mkoa fedha na kuielekeza ku-attend dharura hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Antipas Zeno Mgungusi Mbunge wa Malinyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Malinyi ni kati ya wilaya ambazo ziko chini na hii barabara mvua nyingi zinazonyesha milimani zinapita huko, kwa hiyo kuna changamoto kubwa ya mvua kupita juu ya barabara. Kwa kulitambua hilo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali imeliona na mpango kwanza ni kuongeza fedha kwa maana ya bajeti ili tuweze kuinua hiyo barabara na kuongeza makalavati sehemu ambazo maji mengi yanapita. Ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Barabara ya Lupio – Malinyi- Kilosa kwa Mpepo- Londo mpaka Lumecha ina umuhimu sana sawasawa na ilivyo barabara ya Masasi -Nachingwea - Liwale- Lupilo - Malinyi mpaka Kilosa inaunganisha Mkoa wa Lindi na Mtwara. Nini mkakati wa Serikali kuunganisha kipande hiki cha barabara ili kuwasaidia wakazi wa Mkoa wa Mtwara na Lindi kufika Dodoma kirahisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii iko kwenye mpango wa Serikali kuijenga, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri Serikali inavyopata fedha barabara hii itajengwa ili kurahisisha mawasiliano kati ya Wilaya hizo mbili. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Londo -Lumecha ni muhimu sana lakini inayofanana na barabara ya Londo ni barabara ya kutoka Kilosa mpaka Ulaya kwenda Mikumi.

Je, ni lini Serikali inaenda kuanza ujenzi wa barabara hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilishaanza kujengwa na tuna mpango wa kuendeleza. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ni kuunganisha barabara inayounganisha barabara ya Dodoma – Morogoro kwenda Mikumi ili iweze kujengwa yote kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mipango ipo na bado tutaendelea kuikamilisha hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa sababu changamoto ya barabara kwenye Jimbo la Malinyi inafanana na changamoto ya barabara kwenye Jimbo la Arusha Mjini. Naomba kuuliza swali kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara kutoka kwenye airport ya Kisongo mpaka eneo la Kilombero kwa sababu barabara hiyo inasababisha mafuriko sana kwenye Kata ya Unga Limited, Osinyai na Sombetini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya kutoka Kisongo kwenda Kilombero ni barabara ambayo ipo kwenye mpango na tayari usanifu unaendelea ili kukamilisha na kuweza kuijenga kwa kiwango cha lami na kuondoa changamoto kwa wakazi wa Arusha ambayo wanaipata sasa hivi. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujua ni lini Serikali itatekeleza ujenzi wa Barabara ya Singida- Sepuka-Ndago mpaka Kizaga yenye urefu wa kilomita 95 ambayo imeahidiwa kwenye Ilani zote za Uchaguzi 2015 -2020 na 2020 - 2025 lakini mpaka leo barabara hii haijaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kingu, Mbunge wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoianisha ni kweli imeainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ni azma ya Serikali kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mipango ipo na katika utekelezaji wa Ilani wa miaka hii mitano nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itajengwa kadiri fedha itakavyopatikana. Ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante; je, Serikali itaanza lini ujenzi wa Barabara ya Dareda - Bashnet mpaka Dongobesh kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii iko kwenye mpango na naomba tu tusubiri bajeti kwamba barabara hii Dareda - Dongobesh Serikali ina mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kumekuwa na ahadi ya muda mrefu sana ya ujenzi wa kiwango cha lami barabara ya kutoka njia panda Oldiani-Mangola mpaka Matala Lalago ambayo inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu.

Je, ni lini Serikali angalau hata kwa vipande itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii itaanza kujengwa kwa vipande, lakini barabara itakayoanza kujengwa ni ya Babati kuja Mbulu - Hydom kwenda Sibiti kwa kiwango cha lami na tutaanza sehemu ya Mbulu kuja Hydom na hiyo aliyoitaja tutaanza baada ya muda kwa sababu ni barabara ambayo zinaenda parallel. Kwa hiyo tumeamua tuanze kwanza hii ya Babati – Mbulu - Hydom kwenda Sibiti halafu barabara aliyoitaja itafuata. Ahsante.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Barabara aliyoitaja ya Mbulu- Singida ni tofauti na barabara ambayo ameuliza muuliza swali ambayo inatoka njia panda ambayo inaelekea Mangola ambayo inaelekea Matala ambayo inaelekea Lalago ambayo pia imeunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu. Sasa ni lini Serikali itatoa majibu sahihi ya barabara hiyo kuanza kama alivyotoa majibu ya barabara ya Mbulu-Singida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Awack, Mbunge wa Babati, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ziko barabara mbili ambazo nazifahamu kutokea Babati. Aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge na niliyoitaja ni barabara ambazo zinakwenda parallel na zinakwenda kukutana mbele. Nimesema Serikali imeamua kujenga kwanza Barabara ya Serengeti bypass ambayo inaanzia Babati – Mbulu - Haydom kwenda Sibiti. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kuanzia Ifakara -Kihansi- Madeke mpaka Njombe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum Morogoro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja Serikali itaanza kujenga kadiri fedha itakapopatikana. Ahsante.
MHE. SHABAN O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwanza nishukuru Serikali kwa kututengea fedha za nusu kilomita kwa Barabara ya Magamba kwenda Mlalo na Barabara ya kutoka Magamba kwenda Mlola. Hata hivyo, mara nyingi tumekuwa tukiomba kwamba tuongezewe kilometa tano, je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kilometa tano ambazo tumeziomba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii tumeamua kuijenga kwa awamu na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kupitia Ofisi ya Meneja wa TANROAD wa Mkoa wa Tanga, barabara hii tutaenda kuijenga kwa awamu kadiri fedha zitakapopatikana. Kwa hiyo tutaendelea kuijenga kwa vipande vipande mpaka tukamilishe hizo kilomita tano. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Mheshimiwa Naibu Waziri alikuja kuitembelea Barabara yetu ya Mtwara Pachani - Nalasi na tulitoa ushauri kwamba kuna sehemu ya vipande vipande ambavyo ndivyo korofi vinasababisha watu kulala njiani. Je, Serikali ushauri wetu wa kututengenezea vile vipande korofi wameweka utaratibu gani ambavyo havizidi hata kilomita 10, vipande vile korofi korofi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii nimeitembelea, barabara ambayo ndio inapita kwa wananchi. Mpango wa Serikali kama walivyoshauri Waheshimiwa Wabunge wa Jimbo hasa la Namtumbo na Tunduru tumewaagiza Meneja wa Mkoa wa Ruvuma waweze kuainisha maeneo yote korofi na madaraja korofi ili tuweze kuyatengeneza na kuondoa changamoto ya barabara hii kukatika kupitika kwa mwaka mzima.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Barabara kutoka Kitai-Rwanda-Litui mpaka Ndumbi itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya, Mbunge wa Nyasa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tayari iko kwenye hatua za awali na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi tunakamilisha usanifu wa kina na baada ya kukamilika usanifu wa kina kwa barabara hii ya kutoka Litui kwenda hadi Ndumbi na mpaka Nyasa tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Ikombe, tangu kuumbwa kwa dunia hii hawajawahi kuona gari. Zimebaki kilomita moja na nusu, ili barabara ifunguke mpaka Kijiji cha Ikombe, na mwezi wa kumi tuliambiwa kwamba mkandarasi yuko tayari, amepatikana.

Je, Mheshimiwa Waziri anajua kwamba mkandarasi mpaka sasa hivi hayuko site?

Mheshimiwa Spika, mbili, barabara ya Ngamanga – Lusungo Matema inaenda moja kwa moja Ikombe, pale kuna daraja la bilioni 4.50 lakini eneo la Ngolwa halina daraja. Je, unaonaje sasa ni wakati sahihi wa kujenga daraja la Ngorwa, ili barabara ipitike kirahisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya mheshimiwa Ally Anyingulile Jumbe Mlaghila, Mbunge wa Kyela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wananchi ambao hawajaona gari nimuhakikishie kwamba barabara hiyo tunaifikisha kwenye hicho kijiji ili wananchi hao waweze kuiona gari katika maisha yao.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, naomba nichukue nafasi hii kumuagiza Meneja wa Mkoa wa Mbeya, ahakikishe kwamba mkandarasi anarudi site na anafanya kazi ambayo anatakiwa kuifanya. Lakini kuhusu daraja hili ambalo amelisema, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali italijenga hili daraja ili paweze kuwa na mawasiliano ambayo yamekosekana kwa sasa. Ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini barabara ya kutoka Tanga, Mkumbi, Lugali inayoenda kuunganika na barabara ya Lutoho, Nyasa yenye takribani kilomita 18 itajengwa kwa kiwango cha lami, ikizingatia imekuwa na adha kubwa za kiuchumi kwa wananchi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoainisha ni kweli ipo na imeahidiwa na ipo hata kwenye ilani. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Mbinga, Litembo, Kili ilitolewa ahadi na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nilitaka nijue je, Serikali ina mpango gani wa kuanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunda Mbunge wa Mbinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ahadi zote ambazo zimetolewa na Waheshimiwa viongozi wakuu wa nchi, ni ahadi ambazo tunazitekeleza. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunda, Mbunge wa Mbinga, kwamba barabara hii ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuijenga kama ambavyo viongozi wetu walioahidi na sisi tutamhakikishia kwamba ahadi hiyo tutaitekeleza.
MHE. DKT. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante, wananchi wa Jimbo la Madaba, na wananchi wa Ludewa wamesubiri kwa hamu sana ujenzi wa Barabara ya Mababa – Mkiu – Ludewa kwa kiwango cha lami na hii imekuwa ahadi ya kudumu ya Serikali. Ni lini sasa Serikali itatekeleza azma hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mhagama, Mbunge wa Madaba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mkiu kwenda Madaba ni barabara ambayo inaanzia Itoni, Lusitu, Mkiu kwenda Madaba ambayo ndiyo inaenda kwenye madini ya chum ana makaa ya mawe. Usanifu ulishakamilika kwa kipande cha Mkiu kwenda Luhuu hadi Madaba, Serikali inaendelea kutafuta fedha sasa kuianza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo itajengwa kwa sababu pia ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu ya Tanzania, Ahsante. (Makofi)
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Nataka kujua ni lini Serikali itaanza upanuzi wa barabara kutoka Mpemba mpaka Tunduma – Transfoma ili kuepusha changamoto ambayo wananchi wamekuwa wakiipata kutokana mlundikano na msongamano mkubwa wa magari makubwa ambayo yamekuwa yakivuka mpaka wa Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stella Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Songwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja imeshafanyiwa usanifu na ni sehemu ya barabara ya kuanzia Igawa – Mbeya hadi Tunduma. Na barabara hii kipande cha Mpemba hadi Tunduma kitapanuliwa kuwa njia nne. Kwa hiyo iko kwenye mpango na tunategemea mwaka ujao wa fedha tutaanza kupanua hii barabara kuwa njia nne ili kupunguza msongamano ambao upo katika mji wa Tunduma. Ahsante.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, nauliza je ni lini barabara ya kuunganisha kutoka Mbambay hadi Ludewa itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara inayotokea Mbambay Wilaya ya Nyasa kuja Litui na kuvuka daraja la Luhuu tayari tumeshakamilisha daraja na usanifu umeshakamilika kati ya Mbambay hadi Litui, fedha inatafutwa ili sasa tuanze kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kama tutakwenda na majibu haya mpaka wakati wa bajeti, hali itakuwa tete hapa. Pamoja na hayo naomba kuuliza swali mawili ya nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umekuwa ukifanyika kwa awamu na tayari kipande cha kwanza kimekamilika na kipande cha pili kiko asilimia 81. Serikali haioni sasa ni vizuri kuanza pia ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami, kwa awamu kwa vipande tukianza na bajeti inayokuja mwaka 2022/2023?

Mheshimiwa Spika, Pamoja na ahadi hizo za barabara ya lami, Serikali imekuwa ikijitahidi kutenga fedha kwa ajili ya matengenezo na ukarabati wa barabara hii pamoja na barabara ile ya Korogwe - Magoma kwenda mpaka Maramba. Lakini matengenezo yamekuwa yamekuwa yakifanyika kwa kuchelewa sana lakini pia kifusi kinachowekwa kinakuwa hakina ubora unaoendena na mazingira tuliyokuwa nayo. Na hivi tunavyoongea sasa hivi barabara ya kwa Shemshi haipitiki kwa sababu vifusi havijasambazwa; ni nini kauli ya Serikali juu ya wakandarasi hawa wanaofanya kazi chini ya kiwango na kuwasababishia wananchi wetu matatizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inafanya usanifu wa kina wa barabara hii yote aliyoainisha Mheshimiwa Mbunge, ya kutoka Soni, Bumbuli, Dindira hadi Korogwe ili gharama halisi iweze kufanyika na tuone kama kutakuwa na ulazima wa kuwa na loti moja ama mbili. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa tukishakamilisha usanifu wa hiyo barabara tuona namna ya kuanza kuijenga hiyo barabara; na ni azma ya Serikali kuijenga barabara yote hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, na kuhusu barabara aliyoitaja ya pili, ambayo inaanzia Korogwe, Bombo Mtoni, Maramba hadi Mabokweni, barabara hii inapita kwenye sehemu nyingi ya miinuko. Kwa kawaida arabara kwa kawaida nyingi ambazo zinapita kwenye miinuko zinaoshwa na mvua, tumewaagiza mameneja, wa mikoa waweze kuainisha maeneo yote korofi, ili tutafute namna ya kudhibiti maeneo yote yaliyo bondeni na kwenye miinuko ili tuweze kutafuta utaratibu muhimu wa kuweza kudhibiti hayo maeneo ikiwa ni pamoja na kuweka lami nyepesi ama zege ama strip za mawe ambazo tunahakika barabara hizi zitakuwa na uwezo wa kuitika kwa muda mrefu bila kuitika.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa swali la nyongeza, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri barabara ya kutoka Tambuka Reli, Nyagulugulu mpaka Mahina ni lini Serikali itaanza kuijenga kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFRY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Nyamagana kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeza Mheshimiwa Mabula, amekuwa akija ofisini kuhusu barabara hii. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Nyamagana kwamba Serikali inakamilisha usanifu wa kina wa barabara hii na ina mpango wa kuanza kuijenga barabara hii kwa haraka sana kwa kiwango cha lami kwa sababu kwa watu ambao wamefika Mwanza, ndio barabara pekee ambayo inapotokea changamoto yoyote kati ya Mkuyuni, Igogo kwenda mjini ndiyo inaweza kuwa ni bypass kwa ajili ya watu kufika mjini.

Mheshimiwa Spika kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango wa Serikali ni kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami haraka inavyowezekana.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili.

Swali la kwanza, kutokana na changamoto za kiulinzi zilizopo kwa jirani zetu Msumbiji kuna matumizi makubwa sana ya barabara hii hasa sehemu ya Mahurunga, Kitaya, Mnongodi hadi Mchenjele.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutafuta fedha za dharura na kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami Kilomita 70, wakati tunasubiri fedha nyingi za ujenzi wa Kilomita 358?

Swali langu la pili ni barabara sambamba ni hii ni barabara ya Mnivata Newala hadi Masasi tumeshaambiwa kwamba Serikali imeshapata fedha za ujenzi wa barabara hii.

Je, Serikali inawaambiaje wananchi wa maeneo haya, ujenzi huu utaanza lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunajua barabara hii ni muhimu hasa kutokana na changamoto za kiulinzi katika Mkoa wa Mtwara na Mkoa wa Ruvuma, Serikali mpango wake wa kwanza ni kuifungua yote ili iweze kupitika kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, tukishaweza kwamba inaweza ikapitika na kujenga madaraja yote, Serikali sasa tunaona kutakuwa na haja ya kuijenga kwa kiwango cha lami kwani barabara hii siyo tu kwamba inaishia Masasi pia inakwenda Mkoa wa Ruvuma ambako pia kuna Kilomita 535. Kwa hiyo ni barabara ambayo tunaomba tuifungue kwanza halafu tuanze kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa lami.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusu barabara ya kuanzia Mwinivata, Newala hadi Masasi yenye urefu wa Kilomita 160. Benki ya Maendeleo ya Afrika ilishakubali kuifadhili hiyo barabara na tunapoongea sasa hivi tunachasubiri ni no objection ya hiyo benki, baada ya hapo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge manunuzi yanachukuwa siku 90 ndiyo barabara hiyo itaanza.

Mheshimiwa Spika, hivyo baada ya kupata no objection kutakuwa na mchakato wa manunuzi ambao ni wa kisheria siku zisizopungua 90 na baada ya hapo tutaanza kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, kwa maana ya kuitangaza na kupata Mkandarasi. Ahsante.(Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa hii fursa.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua ni lini Serikali itajenga barabara ya kimkakati kwa kiwango cha lami yenye urefu wa Kilomita 176 inayotoka Kitahi, kupita Amani - Makolo, Paradiso, Rwanda, Lituhi, Mbaha, Lundo, mpaka Mbamba Bay kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ambayo inaanza Kitahi, kupitia Amani – Makolo, Rwanda hadi Lituhi ipo kwenye utangazaji kwa ajili ya kuijenga barabara yote. Kuanzia Kitahi kwenda Mbamba Bay usanifu umeshakamilika na Serikali inatafuta fedha kuijenga barabara hiyo ambayo pia ni sehemu ya barabara ya ulinzi hadi Mtwara. Ahsante.(Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nina swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANROADS ilikuwa na utaratibu wa kujenga kwa kiwango cha lami maeneo ya vilima korofi ili kurahisisha mawasiliano ya barabara hizo.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kwa kiwango cha lami eneo korofi la kilima cha Miyuyu - Ndanda ili kurahisisha mawasiliano ya usafiri kwa wananchi wa Newala wanaoenda kutibiwa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tulishawaagiza Mameneja wote wa TANROADS na kazi hiyo imeshafanyika kuainisha maeneo yote korofi ikiwemo na maeneo haya ya vilima ambavyo viko katika Wilaya ya Newala. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vilima hivyo vitajengwa kwa kiwango cha lami ili isiwe tatizo la wananchi kupata mawasiliano kipindi cha mvua. Ahsante.
MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara inayounganisha Hungumalwa - Ngudu Wilaya ya Magu, imekuwa ikiwekwa kwenye Ilani ya Uchaguzi 2005, 2010, 2015 mpaka 2020 kwamba itajengwa kwa kiwango cha lami, sasa ni lini barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kabula, Mbunge wa Viti Maalum Mwanza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Hungumalwa kwenda Ngudu ipo kwenye mpango na ipo kwenye bajeti kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami kama ambavyo Serikali imeahidi kuifanya. Ahsante. (Makofi)
MHE. KATANI A. KATANI: Mheshimiwa Spika, kutoka Mpwiti, Mkonjoano kuelekea Tandahimba ni barabara ambayo upembuzi yakinifu imeshafanywa zaidi ya miaka minne.

Je, ni lini barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Katani Katani Mbunge wa Tandahimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaji ninataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa usanifu ulishakamilika Serikali inajipanga kutafuta fedha ili iweze kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, azma Serikali ni kuijenga na tuna uhakika itajengwa fedha itakapopatikana. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Nyashimo Wilayani Busega kuelekea Dutwa Wilayani Bariadi imekuwa ikiahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami yenye takribani kilometa 47 kupitia Malili, Dutwa na pale Shigara.

Leo nataka commitment ya Serikali Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya kutoka Nyashimo kwenda Dutwa sasa hivi inafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na itakapokuwa imekamilika barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, ninataka kujua, Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mizani katika Wilaya ya Babati - Kondoa hadi Dodoma.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Sillo Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii amekuwa akiifuatilia sana Mheshimiwa Mbunge, nataka nimhakikishie kwamba kama tunavyomwelekeza na kumweleza kwamba Serikali ina mpango wa kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami kulingana na patikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, katika Ujenzi wa barabara za TANROAD huwa kunakuwa na package ya taa za barabarani kwenye barabara ambazo zimeanza kujengwa kuanzia mwaka 2019. Barabara kutoka Njombe kuelekea Makete ni barabara ambayo ilikuwa ni package ya nyuma.

Je, ni lini Serikali itaingiza package ya taa ya barabarani kwenye Mji wa Handara na Makete Mjini, angalau na sisi Makete tuanze kuona taa za barabarani kama maeneo mengine. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hiyo aliyoitaja ndiyo kwanza inakamilishwa kwa kiwango cha lami na Meneja wa Mkoa wa Njombe ameshatoa tathmini ya barabara, kwa maana ya gharama ambapo tutaweka taa za barabarani Mji wa Ramadhani, Ikonda na Makete yenyewe. Ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, kwa kuwa barabara hii ni ya muhimu sana kwenye utalii wa Serengeti ya Kusini na vipande vya kuanzia Karatu, Mbulu, Haydom, Sibiti mpaka Maswa vimeshafanyiwa upembuzi yakinifu na baadhi ya maeneo yameshaanza kujengwa. Lakini kipande cha kutokea Maswa – Malya – Nyambiti – Fulo havijawahi kufanyiwa upembuzi yakinifu na imekuwa ni ahadi kila mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haioni sasa kwamba kuna umuhimu wa kulichukulia jambo hili kwa ukubwa wake na kufanya upembuzi yakinifu na hatimaye kuijenga kwa lami barabara hii ili watu wa Jimbo la Sumve na Mkoa wa Mwanza na wenyewe wafaidi matunda ya utalii ambayo Serikali imeshaanza kufanya juhudi kubwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa kuwa barabara pacha ya barabara hii ni barabara inayotokea Magu kupitia Bukwimba – Ngudu – Hungumalwa; na barabara hii yenye urefu wa kilometa 71 tumekuwa kila siku tukiizungumza na Serikali katika bajeti inayoisha Juni imepanga kujenga kilometa 10 lakini hakuna dalili zozote za kuanza kujenga.

Je, nini tamko la Serikali kuhusu barabara hii ya muhimu kwa uchumi wa Mkoa wa Mwanza na Wilaya ya Kwimba?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kasalali Emmanuel Mageni, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambayo ameulizia ambayo ipo kwenye swali la msingi nimesema Serikali itahakikisha kwamba kwanza tunaifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kama ambavyo imeainishwa katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo tunaitekeleza. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba kazi hiyo tutaifanya kama ilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lake la pili, barabara aliyoitaja ya Hungumalwa – Ngudu – Magu, barabara hii usanifu wa kina umeshapatikana na ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba mipango ipo na tuna hakika kwamba barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami kama ambavyo tumeainisha. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; barabara ya Singida – Iguguno – Mkarama – Sibiti – Meatu imejengwa kilometa 25 tu, na sote tunafahamu barabara hii ni shortcut kwa watumiaji au wasafirishaji wanaokwenda Mikoa ya Mara na Simiyu.

Sasa ni kwa nini Serikali isitafute fedha kwa udharura wake kuhakikisha kwamba hii barabara inakamilika ile sehemu iliyobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu na ni njia fupi sana, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imejipanga na inaendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba barabara hii sasa tunaijenga na kuikamilisha. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kipande cha barabara ya kutoka Uvinza – Kasulu kupitia Basanza hakina lami, na mara nyingi matukio ya unyang’anyi na ujambazi hutokea katika barabara hiyo ya Uvinza – Kasulu.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja tayari imeshafanyiwa usanifu wa kina na ni barabara kuu ambayo inaunganisha barabara kutoka Mpanda – Uvinza kwenda Kasulu. Sehemu aliyokuwa anaisema ilikuwa inafanyika utekaji tuliamua kuipiga zege ili pawe rahisi kupitika, lakini mpango ni kuikamilisha barabara hii kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwanza naipongeza Serikali kwa ujenzi wa barabara ya Dodoma – Kondoa hadi Babati. Lakini ni lini Serikali itajenga mizani katika barabara hii ili isiharibike ndani ya muda mfupi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara ya Dodoma – Kondoa hadi Babati haina mizani, na ni kwa sababu wakati stadi inafanyika hapakuonekana kama kutakuwa na traffic kubwa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi tunafanya mipango ya kutafuta eneo kujenga mizani ili kuilinda hii barabara ikiwa ni pamoja na barabara ya kutoka hapa kwenda Iringa ambapo napo hapakuwa na lami, tayari tumeshaanza kujenga mizani. Kwa hiyo, Serikali imeshaliona hilo na tuko mbioni kujenga mizani ili kuilinda hiyo barabara. Ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Napenda kuuliza swali kuhusu barabara ya Mlowo – Kamsamba mpaka Utambalila; barabara hii upembuzi yakinifu na usanifu wa kina vimeshakamilika, na mwaka jana nilipouliza swali kuhusu hii barabara Mheshimiwa Naibu Waziri aliniambia kwamba Serikali inatafuta fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu ni hili; je, Serikali bado inaendelea kutafuta fedha au mpango umeishia vipi? Kwa sababu wananchi wa Mbozi wanasubiri kwa hamu sana hii barabara.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa ustawi wa Mkoa wa Songwe. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii baada ya kukamilika kwa usanifu wa kina Serikali inatafuta fedha ili ianze kuijenga kwa kiwango cha lami barabara yote ya kutoka Mlowo hadi Kamsamba, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, barabara ya kutoka Makete kwenda Mbeya ni barabara ya kiuchumi, na katika barabara 16 ambazo Mheshimiwa Rais alisaini zianze kujengwa moja ni barabara kutoka Makete kuelekea Mbeya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mmekuwa mkituambia mko kwenye tendering, tunaomba majibu wananchi wa Makete; ni lini barabara hii itaanza kujengwa ili ifanye ukombozi wa uchumi wa wananchi wa Makete?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Makete – Kikondo kwenda Isyonje ni barabara ambayo ilipata kibali cha kutangazwa na ilitangazwa lakini ilikosa wakandarasi. Barabara hiyo imetangazwa tena na tarehe 22 mwezi uliopita ndiyo ilikuwa mwisho na sasa hivi barabara hii tuko kwenye evaluation ili tujue mkandarasi yupi atapata hiyo kazi.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa hivi tuko kwenye taratibu za manunuzi, tunafanya evaluation ya tender, ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ya kutoka Ilula – Mlafu – Mkalanga – Kising’a hadi Kilolo kwa sasa haipitiki kutokana na uharibufu mkubwa wa mvua.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuiagiza TANROADS kufanya marekebisho ya haraka ili barabara hii muhimu iweze kuendelea kupitika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa ahakikishe kwamba anakwenda kwenye hii barabara ndani ya siku mbili ili kwenda kufanya tathmini na kufanya marekebisho ya sehemu zote ambazo hazipitiki ili wananchi wa Kilolo waweze kuendelea kupata huduma ya barabara hii.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ya kutoka Kiranjeranje – Nanjilinji mpaka Ruangwa ni barabara ambayo Serikali imeahidi kupitia Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020 mpaka 2025 lakini pia upembuzi wa kina umeshafanyika. Lini Serikali inakwenda kujenga barabara hii kwa manufaa ya wakazi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii tumeshakamilisha usanifu wa kina, na haya ni maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya hii hatua ya kukamilisha usanifu wa kina Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza na nishukuru kwa hatua ambazo Serikali imefikia kwa ujenzi wa barabara hii. Pia naomba kujua barabara ya Murushaka kwenda mpaka Murongo, ambayo walishatangaza tender, wamefikia wapi, ili barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Swali la pili; tunayo barabara inayotoka Kyerwa, Makao Makuu ya Wilaya, Nyakatuntu, Kamuli, Kitwe, Mabira mpaka inaunganisha Karagwe; nataka kujua, barabara hii ambayo ni muhimu sana kwa wananchi wetu na ndiyo kuna uzalishaji mkubwa, lakini imekuwa ikijengwa kwa kiwango ambacho siyo kizuri: Ni lini Serikali itaweka barabara hii yote iweze kujengwa kwa changarawe ipitike wakati wote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Omurushaka – Nkwenda - Kyerwa hadi Murongo itaanzwa kujengwa kilometa 50 kati ya Kyerwa kuja Omurushaka kilometa 50. Utaratibu utakaotumika ni kusanifu na kujenga. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii tayari tender ilishatangazwa na mwisho wa kupokea tender ni tarehe 10 mwezi huu wa Tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; nampongeza sana Mheshimiwa Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kwa ufuatiliaji. Kwenye suala hili alilouliza la pili, amekuja ofisini mara kadhaa; na tumekwambia kwamba baada ya kutoa haya maelezo, tumetoa maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kagera ili akaangalie barabara hiyo ili iweze kutengenezwa yote kwa kiwango cha changarawe. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kyerwa kwamba kazi hiyo itafanyika katika bajeti ya mwaka unaokuja. Ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Namanyere – Kirando – Kipili ni barabara ambayo ni muhimu sana kwa ajili ya kukuza uchumi wa Wilaya ya Nkasi na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla. Ningependa kujua ni lini ujenzi wa barabara hii utaanza kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumjibu Mheshimiwa Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara iliyotajwa ya Namanyere – Kirando – Kipili ambayo inakwenda ziwani ni barabara muhimu sana. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tulishafanya usanifu na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili tuweze kuijenga kwa kiwango cha lami barabara hii muhimu sana kwa uchumi wa Tanzania na hasa uchumi wa wana Rukwa na Jimbo hasa la Nkasi Kaskazini. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa naomba kuuliza swali: Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya kutoka Mgungira – Magungumka – Ufana – Mwankalaja kwenda Kaugeri, Mlandara hadi Mwaru? Kwa maana barabara hii imejengwa madaraja kwa kipindi cha miaka 12, mpaka leo madaraja haya hayajakamilika kwa maana ya kujengewa tuta.

Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili TANROADS waweze kukamilisha ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kingu, Mbunge wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba tu Mheshimiwa Kingu tuweze kuonana. Kama barabara imejengwa kwa miaka 12 na haijakamilika, tuweze kuona changamoto ni nini? Nitakuomba Mheshimiwa Mbunge baada ya hapa tuweze kukaa tuone nini cha kufanya kuikamilisha hii barabara muhimu sana kwa Wana-Singida lakini pia wananchi wa Jimbo lako. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; daraja hili ni la muda mrefu sana mimi napenda Serikali itueleze uhimilivu wa daraja hili ni wa kiwango kipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Serikali kutojenga daraja hili ni kuendelea kuwapa adha wasafirishaji wanaosafirisha mizigo zaidi ya tani 10 ambao wanalazimisha kufanya mzunguko kupitia barabara ya Kyaka kwenda mpaka Bukoba Manispaa.

Je, hawaoni kwamba wanaendelea kuwapa adha wasafirishaji hawa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja alilolitaja la Kalebe tunavyoongea sasa hivi mkandarasi yupo anafanya kazi na tunategemea akamilishe mwezi Oktoba japo kwa jinsi anavyokwenda anaweza akamaliza hata kabla. Lengo kuu la kufanya usanifu huu upya ni ili daraja hili liweze kubeba mizigo zaidi ya tani 10 kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera na yapo madaraja mengine pia tunafanya usanifu ili kuyapa uwezo zaidi wa kubeba mizigo tofauti na ilivyo sasa. Ahsante.
MHE: RITHA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, upembuzi yakinifu wa daraja hilo umeshafanyika na wananchi wa Nsimbo wanataka kujua. Je, katika bajeti hii daraja hilo litajengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili. Barabara ya kutoka Kayenze mpaka Kaliua ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati ambayo ameuliza kwa niaba ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo ambaye amekuwa anafuatilia sana ujenzi wa barabara hii. Daraja la Ugalla kama nilivyosema katika jibu la msingi lina urefu wa mita 150 lakini linaunganishwa na madaraja mengine saidizi makubwa zaidi ya matano na makalavati zaidi ya tisa makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Serikali imeanza kuyajenga madaraja hayo saidizi ili tuweze kulifikia hilo daraja kubwa. Kwa hiyo, tayari Serikali imeshaanza kujenga hayo madaraja saidizi na makalavati. Kuhusu ujenzi kwa kiwango cha lami kuanzia eneo la Kawajenzi ambapo ni Mpanda Mjini kupita hilo Daraja la Ugalla hadi Kaliua ujenzi huo utaanza baada ya kukamilisha kuifungua hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, hii barabara ni barabara mpya ambayo inapita katika Mbuga ya Kaliua, upande wa Mkoa wa Katavi tumeshafungua mpaka kwenye daraja lakini upande wa Tabora kwa maana ya kutoka Ugala hadi Kaliua bado tunaendelea kuifungua. Kwa hiyo, baada ya kuifungua tutatafuta fedha kuijenga barabara hiyo sasa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naishukuru pia Serikali kwa majibu mazuri lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza, naipongeza Serikali kwa barabara ya Karatu – Mbulu – Hydom, kipande kinachoanza Mbulu Garbab, kipande cha kilomita 25 taratibu za manunuzi zimeanza tangu Mei, 2021 na hadi sasa haujakamilika. Sasa wananchi wa Mbulu hamu yao ni kuona kwamba barabara hiyo inajengwa.

Je, ni lini taratibu hizo zitakamilika na ujenzi huo uanze?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, barabara hizi nilizozitaja, Barabara ya Dareda, Dongobesh, Kartesh Hydom, Babati Orkesumet kupitia Galapo ni ahadi ya Serikali kwa wananchi wa Manyara ya muda mrefu. Lakini vile vile ni ahadi ya viongozi wa Serikali wakati wa kampeni. Ni barabara ambazo ziko kwenye Ilani ya Chama.

Sasa, ni lini Serikali itaanza rasmi ujenzi wa barabara hizo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi kwa jinsi anavyosaidiana na Wabunge mbalimbali wa Mkoa wa Manyara ambao barabara hizi zinapita kwenye Majimbo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ametaja karibu barabara za mkoa mzima wa Manyara. Mimi nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kipande alichokitaja kwenye swali lake la kwanza la Mbulu Garbab zabuni ilishatangazwa na sasa hivi tuko kwenye hatua ya kusaini mkataba; kwa hiyo siyo hadithi tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipande cha pili cha Garbab Muslur tayari tumeshandaa zabuni na inatangazwa muda wowote. Kwa hiyo tutahakikisha kwamba kipande hiki cha kilomita 50 kati ya Mbulu na Hydom kitajengwa. Kwa barabara zingine alizozitaja ya Hydom - Katesh tayari tulishafanya usanifu wa awali na tunaendelea usanifu wa kina. Dongobesh – Dareda tayari tumeshakamilisha usanifu wa kina.

Vilevile Babati kwenda Galapo hadi Orkesmet barabara hii tunaendelea kuifanyia usanifu ili sasa tuweze kuijenga kwa kiwango cha lami.

Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa wa Mkoa wa Manyara kwamba Serikali iliahidi na hatua zinaendelea kufanyika kuhakikisha kwamba ahadi zinatekelezwa kama zilivyo kwenye Ilani, lakini pia tunajenga hizo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wilaya ya Rorya ni kati ya wilaya ambazo ziko nyuma sana kimaendeleo kutokana na changamoto ya miundombinu. Sasa;

je Serikali haioni kuna ulazima wa kuanza ujenzi wa barabara inayopita Mika, Utegi, Shirati hadi Kirongo; ukizingatia ni muda mrefu sasa, tangu 2017, 2018 ikiwa inafanyiwa upembuzi yakinifu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Agnes Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara aliyoitaja inayoanzia Utegi katika Jimbo la Rorya ipo kwenye mpango wa kufanyiwa usanifu ili ikishafanyiwa usanifu tujue gharama halafu Serikali kama ilivyo kwenye Ilani tuweze kupata gharama na tuanze kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Kwa kuwa barabara ya Ishonje, Kikondo kuelekea Makete kwa muda mrefu sasa imekuweko kwenye bajeti ya kujengwa kwa kiwango cha lami.

Je, ni lini sasa hiyo barabara, hususan kipande cha Ishodye, Kikondo kuelekea Makete, itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Njeza Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekitti, Barabara aliyoitaja ya Ishonje Kikonde Makete ilitangazwa kilomita kama 25 haikupata mkandarasi. Lakini imetangazwa tena ambapo sasa tumeongeza hata kilometa siyo tena 25 ni kilomita kama 50, na ni mwendelezo wa barabara ya kutoka Njombe, Makete kuja Ishondye ambayo inaunganisha mkoa wa Mbeya na mkoa wa Njombe. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari barabara hii imeshatangazwa na ni taratibu tu za manunuzi ambapo tutaanza kuanzia Makete kuendeleza kwenda kuunganisha na mkoa wa Mbeya. Ahsante.
DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi kuuliza swali dogo. Barabara ya kuanzia Kilosa, Lumuma Mpwapwa Ulering’ombe mpaka Ruaha ni mbovu sana.

Je, ni lini angalau itafanyiwa ukarabati kwa kiwango cha changarawe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ishengoma Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara zote za TANROADS zinatengenezwa kwa kiwango cha changarawe. Kwa hiyo nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo katika mwaka huu wa fedha tutahakikisha kwamba tunaitengeneza kama kuna sehemu ina udongo tutahakikisha kwamba tunapeleka fedha ili tuweze kutengeneza barabara hiyo kwa kiwango cha changarawe ili iweze kupitika muda wowote ili kutoa huduma bora kwa wananchi wahusika, ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Wilaya ya Ileje hivi karibuni tumeona namna gani maafa yamekuwa yakitokea kutokana na maporomoko yanayotokea katika barabara ya Ikuti, Sange, Katengele, Kafule mpaka Ikinga. Nilitamani kufahamu ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha barabara hizi zinajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Songwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara alizozitaja za kuanzia Isongole, Ibungu, Katengele hadi Kimo ambayo inaunganisha Ileje na Wilaya ya Rungwe; lakini pia barabara za Isongole, Ibungu, Malangali, Ikinga hadi Kasumulu zinazounganisha Wilaya ya Ileje na Kyela ni barabara ambazo zinapita kwenye miinuko na ni kweli kulitokea maporomoko makubwa sasa mimi mwenyewe nilienda kwasababu zilikuwa zimefunga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kinachoendelea sasa hivi ni kwamba ni kuzifanyia usanifu wa kina barabara ya Isongole, Ibungu, Malangali, Ikinga hadi Kasumulu ili kufanya maandalizi kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Lakini hatua ambazo zimechukuliwa kwa sasa ni kuondoa vile vifusi ili barabara ziweze kufunguka maana yake zilikuwa zimefungwa na nisema tu katika haya maporomoko tulipoteza watu watano baada ya kutokea land slide kwa hiyo unaweza ukaona lakini barabara ya kutoka Ibungu kwenda Tukuyu tutaainisha maeneo korofi ili yaweze kufanyiwa matengenezo maalum na barabara hiyo iweze kupitika kwa kipindi chote cha mwaka, ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa barabara hii ina vipande vingi; je, kipande hiki cha Labay kwenda Hydom na cha Dongobesh kwenda Dareda mnakijenga lini?
Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kipande hiki cha Mbulu kuja Garbabi mmeshamuweka mkandarasi pale na yuko site na hamjamlipa advance payment na hajengi tena barabara;

Je, ni lini mnamlipa advance payment ili ajenge barabara au mpaka turuke tena?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kipande cha Mbulu- Garbabi mkandarasi yuko site, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hajatoka site yupo; na mudo siyo mrefu fedha aliyokuwa anaidai, kwa sababu ilikuwa ni sanifu na jenga, italipwa muda siyo mrefu na kwa hiyo tunaamini kwamba kasi itazidi.
Mheshimiwa Spika, barabara ya Dareda – Dongobesh ipo kwenye hatua za manunuzi na sasa tuko kwenye hatua ya majadiliano na mkandarasi. Ahsante

WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa majibu mazuri. Nilitaka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na wala asiruke sarakasi tena, fedha ile Wizara ya Ujenzi walishaleta maombi yale na tunakamilisha maandalizi tutatoa ile fedha ili mkandarasi asikwame. Na tumeongea na wenzetu wa Wizara ya Ujenzi tutapata majumuisho hata maeneo mengine ambayo yalikuwa na uhitaji wa aina hiyo ili tuweze kukamilisha na kazi zisikwame.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami kilometa 25 katika maingilio ya Daraja la Sibiti ili kunusuru mmomonyoko kwa kuwa barabara iko juu ya mbuga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Daraja la Sibiti linatakiwa kujengwa approach roads, yaani barabara za maingilio kilometa 25. Taratibu za kumpata mkandarasi ambaye atajenga zinaendelea. Hata hivyo bado katika hii barabara ndiyo barabara ambayo mpango wa EPC+F barabara ndefu pia itapita hapo. Ahsante.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini barabara ya kutoka Masasi kwenda Liwale kupitia Nachingwea itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea – Liwale ni kati ya barabara saba ambazo zilichaguliwa kuingia kwenye mpango wa EPC+F; na tunavyoongea sasa hivi upande wa ufundi zimeshakamilishwa ziko kwenye upande wa fedha sasa ya kufanyiwa tathmini.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Karatu – Mbulu kilometa 76 kama ilivyowekwa kwenye bajeti ya mwaka huu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia Issaay, Mbunge wa Mbulu Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom – Sibiti ndiyo barabara ambazo kati ya zile barabara saba ipo kwenye mpango huu wa EPC+F. Kwa hiyo, kama itakavyokuwa imekamilika basi kilometa hizo 76 itakuwa ni sehemu ya ujenzi wa hiyo barabara.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Monduli wamekuwa wakipata changamoto kubwa ya barabara inayotokea Monduli Chini kwenda Monduli Juu nyumbani kwa Sokoine.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga barabara hii katika kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara zote ambazo ni za mkoa zinatakiwa zijengwe kwa kiwango cha lami, lakini kinacho gomba hapa ni bajeti kwa hiyo tunakwenda kwa awamu.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii kwa umuhimu wake pia ipo kwenye mpango lakini itaanza kujengwa pale ambapo bajeti itaruhusu. Ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itaenda kujenga barabara ya Bigwa – Kisaki ya kilometa 78 kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Taletale, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara ilishatangazwa kwa ajili ya kuijenga na kwa hiyo sasa hivi ipo kwenye hatua ya manunuzi kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Barabara ya kutoka Haydom mpaka Katesh ni mwendelezo wa barabara ya kutokea Fulo au Bujingwa kupitia Nyambiti mpaka Mari ambayo imekuwa ikiahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami na Serikali kwenye ilani mbalimbali za uchaguzi; je, ni lini sasa barabara hii inaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, kama nilivyosema barabara hii iko kwenye mpango wa kuijenga; kwa hiyo mara fedha itakapokuwa imepatikana barabara hii sasa tutaanza kuijenga kama tulivyoahidi.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wananchi maneno ya usanifu wa kina au upembuzi yakinifu hawayaelewi vizuri;

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Mogitu – Hydom kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, swali lililoulizwa na Mheshimiwa Hhayuma lilikuwa ndilo swali la msingi lililohusu Mogitu – Haydom na nimeshalijibu kwamba tayari mkandarasi yupo anafanya usanifu wa hiyo barabara tujue gharama halafu fedha itafutwe kwa ajili ya kuijenga, ahsante.
MHE. SEIF K. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa lami barabara ya Choma – Ziba – Nkinga – Simbo mpaka Puge?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Choma – Puge ni barabara ambayo Mheshimiwa Mbunge amekuwa anaifuatilia sana. Hata hivyo, kwa kuwa bajeti bado hatujaiwasilisha naomba Mheshimiwa awe na subira tuone nini mwaka huu tutakuwa tumeipangia hiyo barabara.
MHE: DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza maswali la nyongeza. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itaanzisha mchakato huo ili kuwasaidia kuchochea biashara ya ujirani mwema inayofanyika katika Kijiji hiki cha Kibuye katika Kata ya Kumsenga? (Makofi)

Mheshimiswa Spika, swali la pili; kwa kuwa Mto huo unatenganisha takribani vijiji sita vya Jimbo hili la Muhambwe na wananchi wanapita mipaka holela, je, Serikali haioni iko sababu ya kuharakisha mchakato huu wa daraja ili kuwe na mahali maalum pa kupita hili kudhibiti vitendo vya uhalifu katika Jimbo hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe, kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja hili halipo na linaunganisha nchi mbili, kwa hiyo ni daraja ambalo litahusisha wadau wengine si tu Burundi na Wizara ya Ujenzi, pia itahusisha Taasisi nyingine kama Ulinzi na Usalama, TAMISEMI, Ardhi, Wizara ya Fedha na Mambo ya Nje. Kwa hiyo, wadau wote hawa watakapokuwa wameona kuna haja thabiti ya kujenga na kuona inakidhi vigezo na sisi tukajiridhisha kama nchi, ndiyo tutaanza sasa kuwasiliana na wenzetu wa Burundi. Kwa hiyo sisi tumeshaanzisha huo mchakato kwa upande wetu kuona vigezo vyote vinakidhi, halafu tuweze kuwahusisha wenzetu wa Burundi, ahsante.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya muuliza swali.

Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itakamilisha Barabara ya zamani kutoka Picha ya Ndege mpaka Mlandizi ili kupunguza foleni katika Barabara ya Morogoro?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Barabara ya Makofia - Mlandizi ni barabara ambayo ipo katika Ilani ya Chama kwa miaka mingi Je, ni lini Serikali itaanza kulipa fidia kwa wananchi wanaoishi katika maeneo haya kwa ajili ya maandalizi ya ujenzi wa hiyo barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mpango ni kuiboresha na kuipanua barabara mpya ambayo tunayo, kwa sasa tutaanza kufanya hiyo kazi ya kujenga barabara hizo nne badala ya kuanza na ile barabara ya zamani aliyotaja Mheshimiwa Mbunge. Nadhani kwa kufanya hivyo tutakuwa tumepunguza msongamano ambao upo na ndiyo lengo kubwa kuijenga ile barabara kwa njia nne zinazokwenda, zinazorudi lakini pia na zile zilizopo zitaendelea kuwepo.

Mheshimiwa Spika, suala la pili la Barabara ya Makofia – Mlandizi, Serikali sasa hivi inatafuta fidia ili kuwafidia wale wananchi ambao walishatathminiwa ambapo tuta-review tathmini na kuanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Barabara ya Makambo – Songea barabara kubwa ya kiuchumi ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza na Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tayari imeshapata fedha kutoka World Bank ambapo tutaanzia mbele ya Njombe kuelekea Songea na kipande cha Njombe kuja Makambako Serikali inaendelea kutafuta fedha. Kwa hiyo sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya kuanza kuitangaza ili ianze kujengwa kwa maana ya kukarabatiwa upya total rehabilitations, ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuweza kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Njombe – Itoni, watu bado hawajalipwa compensations nilipenda kujua lini watalipwa fidia wakazi hao? Lakini kibaya zaidi Mawengi – Mlangali tayari barabara imejengwa lakini kuna baadhi ya watu bado hawajalipwa fidia lini watalipwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili naomba kujua barabara ya Makete – Mbeya mkandarasi ameisha saini mkataba lakini mpaka hivi sasa tunavyozungumza hajafika site lini atafika site na ujenzi wa barabara hii ukaendelea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema William Mgaya Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi ambao ameuliza kwamba hawajalipwa fidia kwa eneo la Mawengi – Mlangali nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeisha andaa na kukamilisha Jedwali la malipo ya hao watu wenye fidia wa Mawengi pamoja na hawa wa Itoni – Lusitu na zoezi la kuwalipa nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge litafanyika muda si mrefu.

Mheshimiwa Spika, nakuhusu suala la barabara ya Makete – Isyonje mkandarasi alishapatikana ameisha onyeshwa site lakini kinachosumbua kwasasa kuanza yupo kwenye mobilizations ni hali halisi ya hewa kwa maana ya mvua nyingi inayoendelea lakini tayari mkandarasi ameishapatikana na ameisha kabidhiwa site, ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa usanifu wa ujenzi wa barabara ya Kenyatta kutoka Mwanza Mjini kwenda Buhongwa – Usagara na Airport – Nyanguge zimeishakamilika ni lini ujenzi huu utaanza mara moja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula Mbunge wa Nyamagana kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali hazma yake ni kuijenga hii barabara na kuipanua lakini tayari tumeisha kamilisha usanifu na sasa hivi tunaendelea kutafuta fedha. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge avute subira kwa sababu ndiyo tunaelekea kwenye bajeti tuone Serikali imepanga nini kwenye hiyo barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na kupitisha kwenye bajeti hii inayoendelea lakini bado barabara ya Mafinga – Mgololo na Mgololo – Mtwango hazijaanza kujengwa. Je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara hizi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Kihenzile Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilipangiwa bajeti. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Jimbo la Mufindi Kusini kwamba tayari mkandarasi alishapatikana na kinachomsumbua pia kuanza hii kazi ni kwa sababu tu ya hali ya hewa na Mheshimiwa Mbunge nilishamuhakikishia yeye mwenyewe kwamba tayari tumeisha mpata mkandarasi na tayari ameishaandaa vifaa lakini hawezi kuanza kwa kweli ujenzi kwa mazingira ya Jimbo lake lina mvua nyingi sana lakini mara tu mvua itakapokatika mkandarasi ataanza kujenga kwa kiwango cha lami kwa bajeti ambayo tulikuwa tumeipanga kwa mwaka huu unaoendelea, ahsante sana.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa spika, ahasante sana, kwa kuwa marudio ya upembuzi yakinifu wa barabara inayotoka Bulyanhulu kwenda Kahama umekamilika, vikao vya tathimini vimekamilika, vikao vya Kata zote vimekamilika, fedha zipo cash.

Ni lini sasa Wizara itaanza ujenzi wa barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Idd Kassim Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Bulyanhulu kwenda Kahama kama alivyosema nikweli usanifu ulishakamilika na fedha ipo sasa hivi kinachoandaliwa ni makabrasha tu kwa ajili ya kuanza kuitangaza hiyo barabara ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kusaidiana na wenzetu wa Twiga kwa maana ya Barrick, ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niulize swali la nyongeza. Barabara kutoka Mji wa Namanyere – Bandari ya Kipili ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja amekuwa anaulizia mara kwa mara na mwaka huu tuliipangia fedha na tulishawaambia mameneja wa Mkoa watangaze kwa gharama ile ambayo imepangiwa ili ianze kujengwa hata kama itajengwa kilomita moja, mbili lakini wazitangaze. Kwa hiyo, nataka nichukue nafasi hii kumkumbusha meneja wa Mkoa wa Rukwa aweze kufanya kama alivyopokea maagizo ya kuzitangaza hizi barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, barabara ya Handeni – Kiberashi – Singida ni barabara muhimu sana na barabara hii nashukuru mkandarasi alikwisha ripoti site lakini kinachoendelea sasahivi ni kwamba kama vile kazi aiendelei Je, tatizo liko wapi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kigua Mbunge wa Kilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri wiki iliyopita nimetembelea barabara hii kuangalia changamoto ni nini? Mkandarasi yupo site ameishaanza kazi anakamilisha majengo ya Muhandisi mshauri na kulikuwa na changamoto ndogo ambazo tumeisha zi-sort out na tayari nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuanzia wiki inayoanza hii kasi itaongezeka kwa hiyo barabara inaendelea. Ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante, barabara ya Dareda – Dongobesh – Usariva usanifu wa kina umeishafanyika na zabuni kutangazwa Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo Mbunge wa Babati Vijijini kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara imeishatangazwa na ipo kwenye hatua ya manunuzi kwa hiyo, sasa hivi kuna majadiliano yanayoendelea na mkandarasi ambazo ni taratibu za kawaida za manunuzi. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge barabara hii mara tutakapokamilisha hayo majadiliano mkandarasi tukishakubaliana atakabidhiwa site ili aendelee na ujenzi, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kujenga barabara kwa kiwango cha lami katika Wilaya ya Tunduru ambapo taasisi zote za Serikali zipo katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kungu Mbunge wa Tunduru Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ni barabara za TANROADS zinapita tuna mpango wa kuhakikisha katika kila Miji hasa ya Makao Makuu ya Wilaya, ambapo barabara zetu zinapita basi zijengwe kwa kiwango cha lami. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge mara baada ya hapa tuweze kuonana kama barabara zetu zipo zinapita katikati ya taasisi hizo ambazo amezisema ili tuweze kuona utaratibu wa namna ya kuzijenga kwa kiwango cha lami katika hayo maeneo aliyoyataja, ahsante.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwakunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Kibiti – Dimani – Mloka iko ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM); je, lini Serikali wataanza mchakato wa kuitengeneza barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Twaha Mpenbenwe Mbunge wa Kibiti kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema ipo kwenye Ilani na Serikali kwakweli inaendelea kutafuta fedha kwa barabara hii ili iweze kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwetu tuna barabara ya Mtwara – Pachani – Mkongo – Lusewa – Magazini – Nalasi na Mheshimiwa Naibu Waziri ulikuja kuitembelea na ina hali mbaya sana mpaka sasa hivi na uliwahaidi wazee wale kwamba itatengenezwa kwa kiwango cha lami Je, unawaeleza nini leo Mheshimiwa Naibu Waziri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulitembelea hii barabara ndefu yenye kilomita 300 tumemuagiza meneja wa Mkoa wa Ruvuma kwanza kuhakikisha anaainisha maeneo yote korofi ili yaweze kupata bajeti wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tumeishaongea na meneja wa Mkoa aangalie maeneo yote ambayo ni korofi ambayo tunaweza tukayadhibiti kwa muda wakati tunatafuta fedha ya kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara ya Chekeleni – Kahe – TPC – na Mabogini iko kwenye Ilani awamu hii na awamu iliyopita na pia ni ahadi ya Viongozi Wakuu wa Serikali. Nataka kujua ni lini Serikali itaanza sasa kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami kama ilivyoahidiwa? Natumaini hatasema kwamba ni mpaka hela ipatikane.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema ni ahadi ya viongozi lakini pia iko kwenye ilani naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga barabara zote ambazo imeziaidi kuzijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na barabara ambayo Mheshimiwa Mbunge wa Vunjo ameitaja.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi barabara ya Utegi – Shilati – Kilongwe yenye kilomita 56 upembuzi yakinifu umekwisha kamilika Mheshimiwa Waziri ni lini sasa barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Chege Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja nikweli ipo kwenye Ilani na imeahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami. Naomba nimuombe Mheshimiwa Mbunge asubiri bajeti hii tutakayosoma tutakuwa tumependekeza nini kuhusu barabara hii ya kutoka Mika – Utegi – Ruari hadi Kirongwe, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona, Barabara ya Nyoni – Mlima mkali wa Mawono – Mapela – Maguu kilomita 25 ipo kwenye Ilani ni lini sasa barabara hii itaanza ujenzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kapinga Mbunge wa Mbinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye miinuko na tunachofanya kwa sasa nikuhakikisha kwamba inapitika kwa muda wote wakati tukifanya hivyo Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuweza kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika ahsante sana, kwanza napenda kushukuru kwa majibu ya mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kufuatia umuhimu wa barabara hii ya Nyoni – Mitomoni kiuchumi Serikali ina mpango gani wa kuanza kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Ruvuma wamekuwa wakilia, wakipiga magoti humu Bungeni kufuatia changamoto kubwa ya kuvuka katika Mto Ruvuma ulioko Mitomoni ili kutuunganisha na barabara ya Likwilifusi – Mkenda. Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza kujenga daraja hili kufuatia kilio kikubwa cha wananchi hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella Martin Manyanya Mbunge wa Nyasa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikweli daraja la Mitomoni ni muhimu sana kwa wananchi wa Jimbo la Nyasa nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tumeishapata mkandarasi na sasa hivi tuko kwenye hatua za mwisho za manunuzi ili mkandarasi aweze kuanza kazi hiyo kwenye kujenga hilo daraja ambalo litagharimu si chini ya bilioni 22. Kwa hiyo, tupo kwenye hatua za mwisho kabisaa za manunuzi kwahiyo daraja hilo litajengwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara hiyo, Meneja wa Mkoa wa Ruvuma alishaagizwa aweze kufanya tathmini, kufanya makadirio ya gharama ambazo zinaweza kuwa kwa ajili ya kuifanyia hiyo barabara upembuzi na usanifu wa kina wa hiyo barabara, ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Omulushaka Kwenda mpaka Mlongo mkandarasi ameshapatikana tangu mwaka jana, lakini mapaka leo mkataba bado haujasainiwa. Tatizo liko wapi ili mkataba uweze kusainiwa na mkandarasi aweze kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Olumushaka kwenda hadi Mlongo tayari mkandarasi alishapatikana, na hatua ambayo imebaki sasa ni hatua ya kusaini mkataba ili mkandarasi aweze kukabidhiwa site; na tutaanza kujenga kilomita 50, ahsante.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante na mimi kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya KIA - Sanya Juu ambayo ilikuwa ni ahadi ya Hayati Mheshimiwa Rais Magufuli?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira tuweze kusoma bajeti yetu. Naamini tutakuwa tumefanya mapendekezo ya nini kifanyike kwenye hii barabara ya KIA - Sanya Juu, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Narabara ya kutoka Nagurukuru, Njenje mpaka Liwale ipo katika Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Je ni lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami ambayo inaunganisha Jimbo la Kilwa Kusini, Kilwa Kaskazini pamoja na Liwale?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabra hii Mheshimiwa Waziri alishaahidi. Aliahidi kwenye kamati lakini pia alimuahidi Mbunge, si tu Ally Kassinge lakini hata Mheshimiwa Kuchauka najua anahitaji sana hii barabara; na jana nimekusikia pia ukiichangia hiyo barabara. Naomba tusubiri bajeti tunayokwenda kuijadili sasa hivi, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabra ya kutoka Simbo kwenda Kalia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mhehsimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge Viti Maalum Mkoa wa Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mhehsimiwa Spika, Barabara ya Simbo – Ilagala - Kalia, ipo kwenye mpango wa kujenga kwa kiwango cha lami. Sasa hivi kitakachofanyika ni kwanza kupitia usanifu uliofanyika. Kitu tunachokifanya sasa hivi ni kwanza kulijenga daraja la Malagarasi ili liweze kupitika badala ya kutumia vivuko, na baada ya hapo sasa tunafuta kuijenga hiyo barabra yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. JOHN M. SALLU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, kwa hiyo wananchi wa Handeni tunategemea hivi karibuni michakato itaanza, nina swali moja la nyongeza.

Barabara itokayo Chalinze mpaka Segera, hasa kile kipande kinachoanzia Manga mpaka Segera zinatokea ajali nyingi sana na kupoteza nguvu kazi kubwa sana ya nchi hii, na sababu kubwa ni wembamba wa barabara na kona nyingi.

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kufanya maboresho kwenye barabara hiyo ili tuweze kuondoa vifo hivi vya wananchi wa kitanzania na majeruhi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa John Marko Sallu, Mbunge wa Handeni Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mhshimia Mwenyekiti, barabara ya Chalinze hadi Segera ni barabara ambazo ni barabara standard kwa maana ina upana wa mita 6.5 kwa maana kila upande mita 3.25 na hizo ndiyo barabara zilizo nyingi. Ninatambua kwamba ni kweli kuna ajali nyingi zinataokea lakini ambacho tumekifanya tumetenga fedha kwa ajili ya kufanya economic study na usanifu wa barabara hiyo kwenye maeneo ya miinuko, kona na kuhakikisha kwamba barabara hii ipanuliwe hasa kwenye maeneo ambayo watu wameongezeka kwenye vijiji na kuongeza upana wa mabega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafanya economic study na feasibility study ambayo tutaanza mara moja kwa ajili ya kupunguza ajali ili watu waweze kuonana kwa umbali, ni barabara ambayo imeinuka sana, ukilinganisha na yaani embankment yake ni ya juu. Kwa hiyo, hilo tumeshaliona na Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kufanya hiyo study na economic study. Ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Kibosho Shine, Kwa Raphael hadi International School kwa kiwango cha lami kwani ni kipande kidogo kimebakia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema kipande kilichobaki kidogo nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua kazi kubwa imeshafanyika na tunatafuta fedha kuweza kukikamilisha hicho kipande kilichobaki cha barabara ili wananchi waweze kupata huduma ambayo imekusudiwa na Serikali. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga au kuboresha barabara inayotoka Chuo cha Diplomasia Kurasini kupitia Tom Estate kupitia Msikitini ka Mzuzuri mpaka kuunganisha na barabara ya Mandela? Kipande hicho ni korofi, makontena yanapita kwa shida sana ukiwa na gari ndogo unaweza ukafikiria sasa kontena linaniangukia, nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri tu kwamba sijaielewa vizuri hiyo barabara aliyoitaja lakini nimuombe pia Mheshimiwa Mbunge, kama ataridhia basi niweze kukutana naye ili niweze kuielewa hiyo barabara ili niweze kumpa hasa majibu sahihi badala ya kujibu tu. Sijaielewa vizuri hiyo barabara, ahsante.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumWuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, hiyo barabara ya Iringa Bypass ni mwaka wa tatu sasa tangu imejengwa na imeanza kubomoka.

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Iringa Bypass?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jesca Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii yenye urefu wa kilometa saba tumeshaanza kuijenga. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Iringa na watu wote wanaopita hiyo barabara, Serikali inatambua ni barabara muhimu sana kwani, pale kwenye barabara pakifunga, hatuna njia. Namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira, kwenye bajeti hii tuna hakika tutaendelea kuijenga kwa awamu ili tuweze kuikamilisha na tuwe na barabara ambayo ni bypass kwa Mji wa Iringa, ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera ya Wizara hii inaelekeza kuunganisha barabara ya Mkoa mmoja na Mkoa mwingine kwa kiwango cha lami. Tuna barabara mbili kutoka Karatu kwenda Mbulu ambapo ni Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Arusha; na kuna barabara inayotoka Karatu – Njiapanda – Mang’ola – Lalago ambayo inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu, zote hizi hazijajengwa kwa kiwango cha lami: Je, lini Serikali mtakamilisha barabara hizi au mtajenga barabara hizi kwa kiwango cha lami ikiwa sera yenu inaelekeza hivyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Paresso, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli sera ni kuunganisha barabara kwa kiwango cha lami Mkoa na Mkoa, lakini kipaumbele pia ni kuhakikisha kwamba, kama barabara ambazo zinakwenda parallel tutaanza na moja halafu itafuata nyingine kulingana na upatikanaji wa fedha. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara ya Oldeani – Mang’ola kwenda Matala - Sibiti inakwenda kama parallel, yaani sambamba na barabara ya Karatu –
Mbulu – Hydom – Kidarafa hadi Sibiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo barabara ambayo tunaita Serengere Southern Bypass imeingizwa kwenye mpango wa kuijenga kwa EPC + F, lakini Serikali inafikiria kuijenga barabara kuanzia Oldeani hadi Mang’ola kwa kiwango cha lami kabla ya kupita Mang’ola kwenda Sibiti, ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Serikali iliahidi kuanza kujenga barabara ya Mafinga – Mgololo ambayo ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa letu. Tunashukuru kwa sababu, tayari wamesema itaanza kujengwa: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali ni: Je, ni lini mchakato wa EPC + F utakamilika ili barabara ya Mafinga – Mgololo ianze kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Mafinga kwenda Mgololo imeingizwa kwenye Mpango wa EPC + F. Kama Wizara, upande wa ufundi kwa maana ya engineering, yaani Engingeering Procurement na Construction, tumeshakamilisha, na sasa ziko zinachakatwa na Wizara ya Fedha, na baada ya hapo basi taratibu zinazofuata za manunuzi zitaanza, ahsante.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii. Swali langu kwa Wizara ni kwamba, Mkoa wa Mtwara na Barabara yake ya kiuchumi kilometa 210 kutoka Mtwara – Tandahimba – Newala – Masasi ambayo tayari imeshajengwa kilometa 50 na fedha zimeshapatikana kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika muda mrefu, lakini kila tukiuliza tunaambiwa Serikali ipo kwenye mchakato wa manunuzi. Sasa tunataka kujua, ni lini mchakato wa manunuzi utakamilika ili barabara hii ya kiuchumi ianze kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Newala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara ya Mnivata – Tandahimba – Newala hadi Masasi, kilometa 160 ipo kwenye taratibu za manunuzi. ADB wameshakubali, tumepata no objection; kwa hiyo, kinachoendelea sasa hivi ni taratibu za kawaida za manunuzi na hasa tunapokuwa tunashirikiana na wenzetu wahisani kwamba, tutakapokamilisha lot hizi mbili, zitaanza kujengwa. Tuna uhakika kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha huu, shughuli nyingi zitakuwa zimeanza katika hiyo barabara, ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kuuliza: Je, ni lini sasa Serikali itamaliza ujenzi wa barabara ya Chang’ombe inayoanzia mataa ya Chang’ombe kuelekea barabara ya Kilwa; ukilinganisha kwamba, sasa hivi kuna foleni kubwa sana na ile barabara ni kubwa na hasa ukizingatia wananchi wengi wanapita; na hasa kipindi ambacho kuna michezo kwenye uwanja ule wa Taifa, hasa Simba na Yanga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Chang’ombe kwenda Kilwa ni sehemu ya barabara za BRT Awamu ya Pili. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, naye atakuwa shahidi kwamba kasi imeongezeka sana. Tuna uhakika, kwa mujibu wa kazi anavyoendelea mkandarasi huyu, barabara hii itakamilishwa kama tulivyokubaliananaye kwenye mkataba, ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa majibu ya Serikali, swali langu lilisema ni lini? Sasa Serikali wanasema wapo kwenye hatua za kukamilisha utaratibu wa financial. Sasa nataka kufahamu, huu utaratibu wa financial utakamilika lini ili kuweza kutoa pesa kwa ajili ya kujenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami kwa sababu Wilaya ya Nachingwea na Wilaya ya Masasi na Wilaya nyingine pale hazijaunganishwa kwa muda mrefu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kuna barabara ambayo pia inaendelea kujengwa kwenye eneo hilo hilo kati ya Nanganga – Ruangwa, inaunganisha hizo Wilaya mbili, lakini jengo la Chama cha Mapinduzi, Ofisi ya Kijiji, Msikiti pamoja na majengo ya wananchi mbalimbali yalivunjwa sawa sawa na hii barabara ninayoisema ya Nachingwea – Masasi: Ni lini Serikali italipa fidia kwa watu hawa waliopata athari za kuvunjiwa majengo yao kwa sababu ya ujenzi wa barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze na suala la kwanza ambalo pia umetaka nitoe maelezo kwa Waheshimiwa wote. Ni kweli tuna barabara nane ambazo zimeingizwa kwenye mpango wa EPC + F. Katika barabara nane, barabara itakwenda kwa Mpango wa PPP ambayo ni barabara ya Kibaha - Chalinze hadi Morogoro. Hiyo itaingia kwenye PPP na barabara zilizobaki hizo saba ambazo ni pamoja na hii niliyoisoma ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale zimeingizwa kwenye Mpango wa EPC + F.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango huu ni mfumo ambao ni mpya ambapo wakandarasi wanatafuta fedha, wanajenga, halafu Serikali inatafuta utaratibu wa namna ya kuja kuwalipa kwa makubaliano ambayo yatakuwepo. Sasa kuna sehemu mbili; kuna sehemu ya Engineering ambayo ni Wizara ya Ujenzi wanakwenda na wakandarasi wanaangalia, wana-bid, wanaagalia kwa upande wa ufundi na kuona kwamba wamekubaliana, halafu baada ya hapo sasa, wanapeleka hiyo mikataba Wizara ya Fedha ili kuona kama kwa kuingia nao mikataba hiyo Serikali itakuwa imefanya jambo sahihi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni mfumo ambao ni mpya ambao ni lazima Serikali iende kwa umakini sana ili tusije tukaingia kwenye mkataba ambao hatukujipanga vizuri. Kwa hiyo, kuna umakini mkubwa sana ambao unafanyika ili tuweze kwenda na miradi hii mikubwa ambayo kama tutaijenga, basi tutakuwa tumepunguza kero nyingi sana za usafiri. Tumechukua barabara nyingi zile ambazo ni ndefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa idhini yako nitataja barabara chache. Ni Barabara ya kutoka Ifakara – Malinyi – Kilosa kwa Mpepo hadi Namtumbo. Tuna barabara ya Mafinga hadi Mgororo, tuna barabara ya Kongwa – Kibaya hadi Arusha, tuna barabara ya Karatu hadi Arusha, tuna barabara ya Karatu – Mbulu – Hydom hadi Sibiti. Pia tuna barabara ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale; na tuna barabara ya Igawa – Songwe hadi Tunduma. Hizo ni baadhi ya barabara ambazo zimeingia kwenye mpango huu. Kwa hiyo, ukiangalia ni barabara kubwa ambazo tungetamani tuzijenge kwa wakati mmoja kwa utaratibu huu wa EPC +F, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Barabara inayotoka Dodoma kwenda Iringa ina mashimo, yaani haipitiki, ni shida tupu.

Je, Serikali haioni iko haja sasa ya kwenda kufukia tu yale mashimo badala ya kusubiri muda eti ya kuikwangua barabara yote kiasi ambacho itachukuwa muda mrefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ntara, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara ya Dodoma – Iringa ina mashimo lakini atakubaliana nami kwamba jitihada zimekuwa zikifanyika sana za kuhakikisha kwamba yale maeneo ambayo ni korofi yanazibwa na yanaendelea kuzibwa. Nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hizi zina madaraja. Kwanza, ukiangalia madaraja yapo mengi, sasa wakati tunajenga hiyo barabara traffic haikuwa imetegemewa kama ilivyo sasa. Kwa hiyo sasa hivi bado tunaendelea kufanya economic design kuona namna ya kuboresha hiyo barabara kwa sababu sasa imeoneka ni barabara ambayo inapitisha traffic nyingi lakini pia kuna magari mengi makubwa na mazito ambayo yanapita kwenye hiyo barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. TIMETHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ukizingatia kwamba kazi ya upembuzi na usanifu ulikamilika muda mrefu: Ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kuijenga kwa lami barabara ya kutoka Korogwe – Dindira – Bumbuli mpaka Songwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Korogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema ni kweli barabara hiyo ni muhimu na ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tusubiri bajeti tutakayoisoma, naamini kuna mapendekezo ya kuianza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Kilosa kwenda Mikumi inaungana na Mji wa Kilosa ambako kuna uwekezaji wa mabilioni ya hela station ya SGR lakini kipande hiki kimekuwa kimeingia kwenye bajeti kwa miaka mitano mfululizo bila utekelezaji. Sasa kwa kuwa sisi wengine hatujui kuruka sarakasi ndani ya Bunge, ni lugha ipi ambayo unataka tutumie kuwaeleza Serikali barabara hii ni muhimu kutengenezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Londo, Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali ilishaanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami hadi Kilosa na tumetenga na tumeendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kuendelea kwenda Ulaya hadi Mikumi na ni azma ya Serikali kuunganisha hii Barabara ya Morogoro kutoka Dodoma kwenda Morogoro na Morogoro kwenda Iringa kupitia Kilosa hasa tukitambua umuhimu wa hiyo barabara kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafahamu na ndiyo maana imeanza kutenga fedha na hata kwenye kipindi hiki cha bajeti nina hakika hiyo barabara itaendelea kutengewa fedha ili kuijenga japo siyo yote lakini kwa awamu.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, napenda kujua ni lini Barabara ya Omugakorongo kwenda mpaka Murongo itajengwa ukizingatia Wilaya ya Kyerwa haina lami hata kilometa moja ukiachana na lami ya mchongo ambayo iko Nkwena? Nataka kujua ni lini kwa sababu imechukua muda mrefu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya Omugakorongo hadi Murongo tunavyoongea sasa hivi iko kwenye hatua za manunuzi na nina hakika kabla ya kumaliza mwaka huu wa fedha barabara hiyo itakuwa imeanza na nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii itaanza kujengwa upande wa Murongo kuja Omugakorongo ili tuweze kujenga lile Daraja la Mto Kagera ambao unapakanisha sisi na Uganda.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza naishukuru Serikali kwa kuanza kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo lakini kwa kuwa kuna baadhi ya maeneo ambayo barabara hiyo imewafuata wananchi. Je, Serikali inampango gani kuhakikisha kwamba wananchi hao wanapewa fidia stahiki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa barabara hiyo ina urefu wa kilometa 79 na bado haijakamilika upembuzi yakinifu, Serikali inamkakati gani wa kuhakikisha kwamba inakamilisha upembuzi yakinifu kwa kilometa zote zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Jimbo la Vwawa kwamba tayari jedwali baada ya kuhakikiwa la malipo ya fidia kwa wale ambao barabara imefuata liko hazina kwa ajili ya uhakiki na hatua inayofuata sasa ni kwenda kufanya disclosure, yaani kuwaonyesha kila mtu atalipwa nini kwa maeneo ambayo bado. Kwa hiyo, naomba niwahakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi kwamba suala hili linaendelea na watalipwa hiyo fidia yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kukamilisha upembuzi na usanifu tuko kwenye hatua za mwisho kabisa kukamilisha usanifu ambapo ni hiyo Barabara ya Idiwili lakini Mahenge – Hasamba hadi Ileje.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza swali Mheshimiwa Naibu Waziri. Je, ni kweli kwamba miradi ya barabara ile nane aliyoisema kwenye majibu yake ya msingi ikiwemo ya Masasi – Nachingwea itakayojengwa kwa program ya EPC + F ni kwamba haijulikani lini itaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda na barabara hizi zote kwa pamoja na kama Mheshimiwa Mbunge alinisikiliza, hizi ni hatua na ni mfumo mpya. Kwa hiyo, kusema ni lini tarehe itakuwa ngumu lakini tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ya Fedha sasa hivi inapitia kila barabara na kuona kwamba tunafanya tunavyotakiwa ili tutakapoanza kuzijenga hizo barabara tuwe na uhakika kwamba tulichofanya ni maamuzi sahihi na yatakwenda. Kwa hiyo, cha msingi tu ni kwamba ni hatua, ni process ambayo inaendelea lakini tutakapokuwa tumekamilisha upande huu tukishaanza kuitangaza sasa unaweza ukasema sasa baada ya kuitangaza tuna muda huu na huu.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Barabara ya kutoka pale Nyashimo kwenda Dutwa yenye kilometa 47 tumekuwa tukiahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami zaidi ya miaka 10 sasa na kila nikiuliza toka nimekuja hapa Bungeni nimekuwa nikiambiwa kwamba itaanza kujengwa mwaka wa fedha ujao. Sasa naomba kuuliza ni mwaka wa fedha upi barabara hii sasa itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lusengekile, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema lakini kujenga kwa barabara pia kunategemea kwa kweli na upatikanaji wa fedha na mpango wa Serikali kwa kweli ni kuzijenga hizi barabara kwa kiwango cha lami ikiwepo na barabara ya Mheshimiwa Mbunge. Kwa hiyo, tunakwenda kwenye bajeti naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira, kadiri muda unavyokwenda na kadiri tutakapoendelea kupata fedha barabara hiyo itajengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nataka kujua ni lini Serikali itajenga kipande cha Barabara kutoka Mbande Kisewe mpaka Msongola ili kuunganisha Wilaya ya Temeke na Wilaya ya Ilala?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chaurembo, Mbunge wa Mbagala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama tulivyoongea barabara hii imeshakabidhiwa kwa Manager wa Mkoa wa Dar es Salaam kukamilisha hicho kipande kidogo sana ambacho kimebaki kwa kiwango cha lami.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Mbinga – Litembo – Nkili ni barabara muhimu sana kwa wakulima wa kahawa. Nataka nipate majibu ya Serikali ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunda, Mbunge wa Mbinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyotaja itaanza kujengwa mara tu tutakapokuwa tumefanya review ama kukamilisha usanifu wa kina ikiwa sasa tutakuwa tumepata gharama ya hiyo barabara kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa kuwa ipo Barabara ya Makondeko – Kwembe – Kisopwa hadi Mloganzila ya kilometa 14.66 imekuwa kwenye mpango na bajeti kwa miaka mitatu mfululizo. Je, ni lini sasa Serikali itaanza kujenga kipande cha Makondeko kuelekea Kwembe hadi Kisopwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Makondeko – Kwembe kwenda Kisopwa ni kati ya barabara ambazo zimejumuishwa kama barabara za kupunguza misongamano katika majiji. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mpango upo wa kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Jimbo la Geita Vijijini wananchi wake hawajawahi kuona lami na tulipata lami kilometa 20 kutoka Nkome mpaka Kijiji cha Igate na upembuzi yakinifu tayari Mkandarasi tayari.

Je, ni lini mkandarasi huyo anaingia site kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Musukuma, Mbunge wa Geita kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tupo kwenye hatua za mwisho kabisa ili mkandarasi aweze kukabidhiwa hiyo site na nadhani Mheshimiwa Musukuma pia anajua kwamba taratibu zote karibu zimeshakamilika kwa hiyo kilichobaki tu ni hatua za mwisho ili mkandarasi aweze kukabidhiwa hiyo site.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kuniona.

Ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami kwa barabara inayotoka Singida Mjini – Ilongero – Mtinko mpaka Haydom kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ighondo, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Singida – Ilongero inayoelekea Hydom tupo tunakamilisha usanifu wa mwisho. Tulifanya usanifu wa awali lakini sasa hivi tupo tunakamilisha usanifu na baada ya kupata hiyo detail design ndiyo sasa mipango ya kuijenga kwa kiwango cha lami itaanza.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru, nataka nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna barabara ambayo inatoka Mtwara Mnivata inayojengwa kwa kiwango cha lami kuelekea Newala mpaka Masasi. Kwa taratibu ambazo zinaendelea sasa hivi kuanzia Mnivata – Newala – Masasi wapo kwenye hatua za kulipa malipo kwenye zile nyumba ambazo zimeondolewa na miche. Lakini kipande cha kilometa 50 ambacho tayari kimejengwa barabara ya lami mpaka leo wananchi hawajalipwa fedha zao kama fidia. Je, ni lini Serikali itarudi kuwalipa fidia wananchi wale?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi barabara Mtwara – Mnivata imetekelezwa kwa fedha ya Serikali ya Tanzania na Barabara ya kuanzia Mnivata – Newala kwenda Masasi itatekelezwa kwa kusaidiana na wahisani ambao ni African Development Bank.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwamba kama kuna wananchi ambao katika eneo la Mtwara Mnivata bado wana changamoto ikiwa ni nje ya zile kilometa 45 tuweze kuonana nae ili niweze kupata taarifa kamili kwa wananchi ambao bado wanadai fidia eneo hili la Mtwara – Mnivata kilometa 50.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Barabara inayoanzia USA River kupitia Arusha National Park kwenda mpaka Oldonyo Sambu imejengwa kwa kiwango cha lami hadi kwenye lango la kuingia hifadhini.

Je, Serikali inampango gani wa kumalizia kipande kilichobaki kuanzia Ngarenanyuki kwenda Oldonyo Sambu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Arumeru kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, azma ya Serikali ni kukamilisha hicho kipande ambacho kimebaki lakini ukamilishaji wake pia utategemea na upatikanaji wa fedha na kwa kuwa tuko kwenye kipindi cha bajeti naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira tuone kama tutakuwa tumependekeza nini katika bajeti ambayo tunaiendea kuileta mbele ya Bunge lako.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika,
ahsante kwa kunipatia nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nashukuru sana kwa majibu ya Serikali kusikia kuwa barabara ya Mikumi – Kilosa imeanza kufikiriwa na itaanzwa kujengwa, lakini naomba ipewe kipaumbele kwa sababu ni barabara muhimu.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza: Kutokana na msongomano wa pale Msamvu, Morogoro Manispaa, naomba kujua barabara ya bypass ni lini itajengwa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili: Ni lini itajengwa Barabara ya Ubena – Ngerengere mpaka Mvuha kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya bypass katika Mji wa Morogoro ni sehemu ya Mpango wa Express Way ambayo itajengwa kutoka Chalinze hadi Morogoro na iko tayari kwenye usanifu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba itatokea Kingorowira – Makunganya hadi Sanganga eneo la Mzumbe. Kwa hiyo, hilo litaondoa changamoto ambayo ipo katika Mji wa Morogoro kwa maana ya msongamano. Kwa hiyo, tayari Serikali imelifanyia kazi na limeingizwa kwenye huo mpango.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la barabara ya Ubena – Zomozi kwenda Ngerengere, barabara hii ilitangazwa kwanza kwa awamu kilometa 11.6 lakini haikupata Mkandarasi, imetangazwa tena kuijenga kwa kiwango cha lami, na hivi tunavyoongea sasa hivi, tathmini ya zabuni inaendelea kwa barabara hiyo kwa kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini barabara ya Katoke – Nyamirembe itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami, kwani ipo kwenye bajeti ya mwaka huu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhandisi Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja tumeitengea bajeti kwa ajili ya kuanza maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami na tuna hakika kwamba hata katika bajeti itakayokuja tumependekeza hiyo barabara ianze kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wakati Barabara ya Namtumbo – Songea au Songea – Namtumbo inajengwa, Serikali ilifanya tathmini kwa nyumba zilizokuwa karibu na barabara na kuwalipa fedha wenye nyumba hizo zilizobomolewa, lakini leo hii kumejitokeza nyumba zilizokuwa nyuma ya upanuzi wa barabara hiyo zimeenda kuwekewa X na kutakiwa zivunjwe Namtumbo Mjini.

Je, Serikali inaweza kusitisha zoezi hilo mpaka ije ifanye tathmini, nyumba hizo zisibomolewe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nimemwelewa vizuri, baada ya mabadiliko ya sheria, tuliongeza upana wa barabara kutoka meta 45 kwenda 60. Kwa hiyo, kila upande tumeongeza kilometa 7.5 kila upande. Sasa kama suala ni hilo, Serikali inafanya tathmini kwa maeneo yote ili kujua gharama halisi ya wale ambao barabara imewafuata. Kwa sababu walikuwa wamejenga maeneo hayo kisheria, lakini kwa sababu tumeamua tupanue barabara zetu kutokana kuongezeka na kuboresha miundombinu yetu, tunalazimika, na hao watu watalipwa fidia, ahsante. (Makofi)
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii ili nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini sasa Serikali itamaliza kutujengea barabara inayotoka Mayanga kuelekea Mkunwa kwenye Halmashauri yetu ya Wilaya kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shamsia, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja itajengwa kwa kiwango cha lami, na kwa kweli itategemea na upatikanaji wa fedha na kwa kweli sina uhakika kama kwenye bajeti hii imo. Tusubiri hiyo bajeti tuone kama itakuwa ipo kwenye mapendekezo kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Barabara ya kutoka Uvinza mpaka Kasulu itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Uvinza – Kasulu ni sehemu ya barabara kuu ya kutoka Mpanda – Kasulu hadi Nyakanazi na tayari Serikali imeshaanza kuijenga kipande cha Uvinza kwenda Mpanda, na sasa hivi Serikali inatafuta fedha ili kukamilisha kipande hicho ambacho kimebaki takribani kama kilometa 57. Kwa hiyo, tutaikamilisha yote, na tumefunga upande ule wote kuwa barabara ya lami kutoka Nyakanazi – Mpanda hadi Tunduma, ahsante. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kutoka Mlowo – Kilyamatundu – Ilemba – Mtowisa hadi Majimoto kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Rukwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kipande cha Mloo hadi Kamsamba imewekwa kwenye mapendekezo ya bajeti. Pia ilikuwa ni ahadi ya Waziri Mkuu, aliaagiza, lakini upande wa Kilyamatundu hadi Muze tumeshaanza barabara hiyo kutoka Ntendwa hadi Muze kwenda Kilyamatundu. Kwa hiyo, barabara hiyo tumeshaianza na ni matumaini yetu kwamba tutaendelea kuikamilisha. Ni barabara ndefu yenye kilometa zisizopungua 300, ahsante.
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya muda mrefu ya kujenga barabara ya kutoka Rujewa – Madibira mpaka Mafinga yenye kilometa 151? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bahati Ndingo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilitengewa fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Tunaamini pia tutaiweka kwenye mapendekezo ili iweze kuanza kwa ajili ya uzalishaji mkubwa sana wa mpunga katika eneo ambalo hii barabara inapita, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Barabara ya Kolandoto kwenda Kishapu - Mwangongo yenye kilometa 63 ni barabara ambayo sasa imekuwa kero kubwa kwa wananchi wa Kishapu; na barabara hii iko kwenye Mpango wa Bajeti 2022/2023; na iko kwenye Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi; ni lini sasa barabara hii itaanza kutekelezwa rasmi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Butondo, Mbunge wa Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakubaliana naye, lakini hii barabara ni sehemu ya barabara ndefu ambayo tumeitengea bajeti na atakubaliana nami, kwa ajili ya kuanza maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, tuna uhakika barabara hii kwa kuwa iko kwenye mpango na pia ni barabara kuu, Serikali itaijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza: Katika Mji wa Mpwapwa kuna eneo dogo sana ambalo liliwekwa taa zamani, lakini taa hizi muda mwingi hazifanyi kazi: Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati taa hizi ili ziweze kufanya kazi angalau katika eneo hilo dogo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Mheshimiwa Rais amejenga daraja kubwa la TANESCO katika Mji wa Mpwapwa; daraja hili limejengwa katika eneo lenye miti mingi, kwa hiyo, husababisha giza nene wakati wa usiku. Mazingira hayo yanahatarisha usalama wa watumiaji. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri atakubaliana nami kwamba jambo la kuweka taa katika eneo hili ni la dharura lisilohitaji kusubiri taratibu za manunuzi? Kama jibu ni ndiyo; ni lini wataweka taa katika daraja hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, taa tunazoweka ni kwenye Barabara ambazo ni za TANROADS na kilometa 2.5 naamini tutakuwa tumepita pia kwenye maeneo hayo anayoyasema na hata tutayawekea lami na kuweka taa. Kwa hiyo, nina hakika kwa kilometa mbili na nusu tutakuwa tumekamilisha taa katika Mji wa Mpwapwa. Kama kutakuwa na changamoto ya hizo taa, nitaomba Mheshimiwa Mbunge tuweze kuonana ili tulichukue kama ni jambo la namna yake ili tuweze kuangalia kama hizo taa zinarekebishika ama tutaweka taa nyingine.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, kama nimemsikia kuhusu daraja ambalo liko katika Mji wa Mpwapwa; limeshakamilika na tunatambua kwamba kuna mmomonyoko mkubwa ambao unaendelea. Sisi kama TANROADS kwa maana ya ujenzi, linahusisha watu wengi; watu wa mazingira, watu wa bonde la maji, na pia TAMISEMI kwa maana ya kwamba ni wadau. Sisi tunaweza tukajenga lakini kwa kushirikiana na hao wadau, na Mheshimiwa Mbunge tulishaongea naye kwamba Serikali imelichukua kwa wadau wote, tuone namna ya kuweza kudhibiti mmomonyoko ambao unaendelea ambao pia utahatarisha hilo daraja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba liko, linafanyiwa kazi na Wizara zinazohusika kuweza kulijenga hilo daraja, kwa maana ya kurekebisha hizo kingo za daraja la huo Mto Mpwapwa.
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE. Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, ninataka nijue ni lini basi Serikali ina uhakika wa kupata hii (No objection) kutoka kwa Benki ya Maendeleo ya Afrika ili tujue kwa uhakika kabisa ni lini tutaanza utekelezaji wa mradi huu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ninataka kufahamu ni lini Serikali kwa kushirikiana na Halmashauri ya Manispaa ya Wilaya ya Temeke itajenga stendi mpya kwa ajili ya mabasi ya kutoka Mtwara, Lindi na Ruvuma yanayoingia Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya Dual Carriage Way ya kutoka Dar es Salaam kwenda Mkuranga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Geoffrey Mwambe, Mbunge wa Masasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu za manunuzi zinakwenda vizuri na ni matumaini yetu kwamba kama wenzetu watakwenda kama tulivyopanga tunategemea tutapata (No objection) kwa sababu taratibu zote karibu zimekamilika. Sasa ni lini? Kwa kweli tutanategemea wenzetu wa African Development Bank watakavyokuwa wamefanya kazi yao kwa uharaka na kutoa hiyo (No objection) na sisi tutaanza kutangaza hiyo kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kujenga stendi, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi kama wizara kwa kushirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ambao hasa ndio wanaoshughulikia stendi hizi za mijini, tutakaa pamoja tuone uwezekano wa kujenga hiyo stendi na hasa tu nikimhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa upande huo tayari tuna utaratibu wa kuja na mpango wa kujenga dual carriage way ya kutoka Mbagala – Kongowe na ikiwezeka mpaka Vikindu. Ahsante.
MHE. CATHERINE D. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, je, ni lini barabara ya kutoka Waso kwenda Loliondo yenye urefu wa kilometa 10 itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Arusha, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile ilikuwa ni ahadi na agizo la Mheshimiwa Rais, hivi tunavyoongea tayari tenda ilikwishatangazwa ya kujenga kilometa hizo 10 za kutoka Waso hadi Loliondo kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kupata nafasi hii, kwa kuwa ipo ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa stendi ya kisasa katika Mji wa Mwanga, swali langu ni je, ni lini ahadi hii ya Mheshimiwa Rais itatekelezwa kwa wananchi wa Mwanga? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Tadayo aniruhusu niweze kupata maelezo sahihi ya kuhusu utekelezaji wa hii ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa TANROADS kujenga hii stendi ya kisasa katika Mji wa Mwanga baada tu ya kutoka kwenye kipindi hiki. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa barabara ya kutoka Bariadi – Itilima – Meatu – Sibiti mpaka Singida iko kwenye ilani. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara ni sehemu ya Barabara ambayo ni ya kutoka Maswa – Sibiti Kwenda Haidong ambayo ipo kwenye mpango wa EPC+F na nimekwisha itolea maelezo mengi kwamba tayari taratibu zinaendelea na sasa tayari upande wa Wizara ya Ujenzi tumemaliza sasa tumekwishapeleka kwa wenzetu Wizara ya Fedha kuweza kupitia mapendekezo yetu. Ahsante.
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Mwenge kuelekea Bagamoyo imekuwa na msongamano mkubwa na kusababisha Shughuli za kiuchumi Mkoa wa Dar es Salaam kusimama. Ni lini sasa Serikali itajenga barabara ya Mabwepande kuelekea Mbezi Jimbo la kibamba ili kuweza kupunguza foleni hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara ya kutoka Mwenge kwenda Mabwepande ni BRT number Four ambayo iko katika hatua za manunuzi, lakini barabara aliyoitaja itakuwa ni moja ya barabara za kupunguza msongamano lakini pia kwenda kwenye hii stendi mpya na iko kwenye mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunpa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa wananchi hawa wamesubiri muda mrefu, wamepisha barabara hii takribani sasa tokea 2012 ina maana sasa hivi takribani miaka 11 mpaka leo hawajapata fidia zao na kuna wengine wamefariki. Je, kupitia hii kero Waziri yuko tayari kuja kuzungumza na wananchi wa Kata ya Sitalike?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa hii imekwisha kuwa shida. Je, Serikali inajipangaje sasa kupitia tatizo hili la fidia kuhakikisha kabla hawajawatoa watu wahakikishe wamewalipa kwanza ili isiwe kero kupitia Serikali?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo yote kwa pamoja kwa ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la fidia hasa kwa mita 7.5 limekuwa linajitokeza mara kwa mara, na mimi napenda tu nitumie nafasi hii kuwajulisha Waheshimiwa Wabunge kwamba hii ni Sheria ya kuongeza upana wa barabara kutoka Mita 45 kwenda mita 60 ya mwaka 2007. Kufanyika huku kulikuwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na hifadhi kubwa ya barabara ili tunapotaka kufanya shughuli zozote ikiwa ni pamoja na kuongeza upana wa barabara ama kupitisha mifumo mingine yote iwe ya maji, ya mikongo ya mawasiliano tuweze kuwa na hifadhi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ilikuwa ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na hifadhi kubwa ya barabara ili tunapotaka kufanya shughuli zozote, ikiwa ni pamoja na kuongeza upanda wa barabara, ama kupitisha mifumo mingine yoyote iwe ya maji, na mikongo ya mawasiliano, tuweze kuwa na hifadhi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tutakuja na taarifa sahihi ya utaratibu ambao tutaufanya kwa sababu ni nchi nzima ambapo tumeongeza huo upana wa barabara, namna bora na sahihi ya kuweza kuchukua hayo maeneo na kuwalipa fidia, ama kama kutakuwa na maelekezo mengine ambayo Serikali itakuja kuyatoa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Anna Lupembe pamoja na Wabunge wengine wote ambao wana changamoto hizo kwenye majimbo yao kwamba, Serikali itakuja na utaratibu mzuri wa namna bora ya kufidia wananchi ambao barabara imewafuata, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa wananchi waliopisha barabara ya Bypass ambayo ni mpya ya Uyole mpaka Songwe?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyotaja Mheshimiwa Njeza Mbunge wa Mbeya Vijijini, ni mpya, inajengwa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zinaendelea na barabara ambazo tunazijenga wananchi watafanyiwa tathmini na wakati tunaanza ama kabla hatujaanza, wananchi hawa watalipwa fidia zao, ahsante.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wa Ngoni, Himiti, Singe hadi Komoto ambao wamepisha ujenzi wa Bypass katika Mji wa Babati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Regina, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika majibu mengine, ni kwamba wananchi hawa wameshafanyiwa tathmini na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuweza kuwalipa fidia yao wananchi ambao wamepisha mradi huu wa barabara wa Bypass katika Mji wa Babati, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa kuwa mradi wa bypass unaanzia Kata ya Kisaki - Nyamikumbi - Unyambwa mpaka Utipa umeshafanyiwa upembuzi yakinifu: Ni lini ujenzi huu utaanza?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilishafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa Bypass ya Singida. Kitakachofanyika sasa ni kufanya mapitio upya na kupata gharama ya sasa ya ujenzi. Kwa hiyo, barabara hii baada ya fedha kupatikana tutaanza kuijenga ili kupunguza msongamano katika Mji wa Singida, ahsante. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Serikali imekuwa na changamoto kubwa sana ya ulipaji wa fidia kwa wananchi wanaopisha miradi mbalimbali ya maendeleo. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kufanya tathmini baada ya kuwa mmepata fedha ili kuondoa usumbufu kwa wananchi ambao wanapisha miradi kwa hiari?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofanya miradi ya barabara, fidia inakuwa ni sehemu ya gharama ya ujenzi wa hiyo barabara. Kwa hiyo, tunapokuwa tunafanya ujenzi ni pamoja na fidia. Kwa hiyo, tunaposema gharama ya barabara hii, ni pamoja na fidia ya wananchi ambao wanapisha hiyo miradi, ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa ya swali dogo la nyongeza. Kutokana na mvua kubwa inayonyesha Bonde la Ziwa Rukwa, madaraja takribani sita yamesombwa na mafuriko: Je, ni lini kauli ya Serikali juu ya kurudisha mawasiliano kwa dharura katika eneo hili la Bonde la Ziwa Rukwa ambalo na Mheshimiwa Naibu Waziri unalijua fika?
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sangu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba katika kipindi cha mvua, barabara nyingi huharibika na madaraja mengi kusombwa likiwemo daraja la Mheshimiwa Sangu ambalo ni eneo la bondeni. Naomba tu nichukue nafasi hii kumjulisha ama kumpa maelekezo Meneja wa TANROADS Mkoa wa Rukwa ahakikishe kwamba anapeleka timu ya wataalam kuanza kufanya tathmini na ikiwezekana kurudisha mawasiliano ya muda na pia aweze kuleta taarifa Makao Makuu kuomba uwezesho wa fedha ili kurejesha mawasiliano haya ya kudumu, ahsante.
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina swali la nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, katika tengo la fedha hizi, je, Serikali itaweka pia na huduma ya taa za barabarani kwa sababu, barabara hii imekatiza katikati ya mji?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, ni mpango sehemu tunapojenga barabara za lami mijini tunaweka na taa. Na Mbunge atakuwa shahidi kwamba, mpaka sasahivi tumeshaanza kuweka taa za barabarani katika mji wa Kondoa.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa fursa hii. Naomba kuuliza swali la nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, je, ni lini barabara ya kutoka Itilima kwenda Meatu itajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja Mheshimiwa Sabu, Mbunge wa Viti Maalum, Simiyu, ipo kwenye mpango na ndio maana sasa hivi tunachofanya ni kufanya review ya usanifu, ili Serikali iweze kujua gharama yake kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika barabara ya Njia Nne hadi Kipatimu tayari Serikali imejenga kilometa 1.9 za lami. Je, Serikali ina mkakati gani wa kukamilisha kilometa zilizobaki katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuikamilisha hiyo barabara kwa kiwango cha lami, lakini tutakwenda kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili. Swali la kwanza; je, Serikali iko tayari sasa kuongeza fedha 2023/2024, walau kuanza kilometa 10 za barabara hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kilometa nane kwa ajili ya ujenzi wa Barabara ya Dareda – Dongobesh imetangaza zabuni mwezi Machi, sasa ni lini kazi hii itaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara hii ya kutoka Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu tumeshaanza kuijenga kwa kiwango cha lami kwenye maeneo ya escarpment na tutaendelea. Tumeshajenga kilometa nne lakini pia tumetenga fedha ili kuendelea kujenga eneo hilo la muinuko mkali kwa kiwango cha lami wakati Serikali sasa inaendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote ya Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Barabara ya Dareda – Dongobesh, tulitangaza tenda wakandarasi wakakosa sifa. Tumetangaza tena na sasa hivi tupo kwenye evaluation. Ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Barabara ya kutoka Iringa Mjini kwenda katika Hifadhi ya Taifa Ruaha ambayo imetengewa fedha miaka mingi lakini hazitoshi na hazitoki na upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishafanyika; je, ni lini sasa hii barabara itakwenda kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Barabara ya Iringa – Ruaha (Iringa Msembe), kilometa 104, inafadhiliwa na World Bank na hivi tunavyoongea iko kwenye hatua ya manunuzi kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Je, ni lini eneo la Nyangoye katika Barabara ya Uganda – Bukoba Mjini litarekebishwa, ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais, ili kuondoa ajali zinazotokea mara kwa mara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Kagera, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, lilikuwa agizo la Makamu wa Rais na sasa hivi kinachoendelea ni kufanya usanifu wa namna ya kuijenga barabara hiyo. Ahsante.
MHE. SANTIEL E. KIRUMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Barabara hii imekuwa ikiahidiwa na viongozi wengi wakubwa wa Serikali tangu mwaka 2010 na haijatekelezwa mpaka sasa kwa kilometa hizo 148 kwa kiwango cha lami. Nini kauli ya Serikali kuikamilisha barabara hii kwa sababu imekuwa kero kwa watumiaji wake?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni lini pia Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami kutoka Kahama – Nyandekwa – Nyamilangano (kilometa 148)? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Santiel Kirumba, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Mwanangwa – Mwakitolyo
– Bulige hadi Kahama ni kweli imekuwa ikiahidiwa na ndiyo maana tumeanza kuijenga kwa hatua na hasa maeneo ambayo tunajua ni ya mjini wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nia ya Serikali ipo na ndiyo maana tumefanya usanifu barabara yote na tumeanza kujenga maeneo yale muhimu kwa hatua tukitafuta fedha yote.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa barabara aliyotaja ya pili kutoka Nyandekwa – Wogo, barabara hii ipo kwenye mpango na tumeipangia fedha kwenye mwaka huu wa fedha ikiwa ni maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa Barabara ya kutoka Old Shinyanga kwenda Iselamagazi mpaka Solwa ni barabara ambayo inaunganisha Manispaa na Shinyanga DC.

Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii tumeshaanza kuijenga kwa awamu na tunahakikisha kwamba tayari tumeshafanya usanifu na tutaijenga kwa kiwango cha lami ili kuunganisha Makao Makuu ya Mkoa wa Shinyanga na Halmashauri ya Shinyanga Vijijini. Kwa hiyo mpango upo kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara ya Kiberashi – Chemba – Singida kandarasi yake imetangazwa lakini kuna kipande cha kama kilometa 18 kutoka Goima hadi Kondoa. Nataka kujua commitment ya Serikali ya kujenga kipande hicho. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Goima – Bicha ni barabara ambayo sasa tumewaagiza Mkoa wa Dodoma waweze kufanya usanifu, maana yake ilikuwa haijafanyiwa usanifu, wafanye usanifu ili iwe ni link kati ya barabara ndefu ambayo tutaijenga ya Kiberashi – Singida halafu hiyo itakuwa ni link. Mwaka huu tumepanga waanze kufanya usanifu ikiwa ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa barabara hii ina ahadi ya muda mrefu; Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari baada ya Bunge hili kwenda Jimboni Lupembe kuwaambia wananchi juu ya ahadi hii nzuri ya Serikali?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili, wananchi wa Nyombo, Kidegembye, Matembwe, Barazani, Madeke na Mfiriga nyumba zao zimewekwa X tangu mwaka 2014. Ni upi mpango wa Serikali sasa kuwalipa fidia wananchi hawa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo nimeshaitembelea. Na kwa kuwa tunaenda kuanza niko tayari baada ya kikao hiki cha Bunge kwenda jimboni kwa Mheshimiwa Mbunge na kuweza kuongea na wananchi, kuwaeleza nini tutakachokifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tulikuwa tumefanya tathmini muda na tayari tumeshamu-engage consultant kwa ajili ya kuhuisha ule uhakiki uliofanyika, ili sasa tuweze kupata taarifa za sasa kwa ajili ya kuwalipa fidia wananchi hawa ambao wote waliwekewa alama za “X” ili tuanze ujenzi.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, barabara inayotoka Handeni kwenda Songe na Kiteto ni siku ya pili sasa hivi haipitiki kutokana na na mvua zinazonyesha, na shughuli zote za uchumi zimesimama. Je, nini kauli ya Serikali juu ya barabara hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kigua, Mbunge wa Kilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwape pole wananchi wa Kilindi kwa adha wanayoipata kwa sababu ya changamoto ya mvua. Napenda nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Tanga aweze kufika maeneo yote ambayo yameathirika na kuweza kurejesha mawasiliano kwa muda, na pale ambapo changamoto itakuwa ni kubwa, basi aweze kuwasiliana na TANROADS Makao Makuu kwa ajili ya kutoa msaada mkubwa zaidi, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Kwa kuwa upembuzi na usanifu wa barabara ya kutoka Kiranjeranje – Makangaga – Nakiu – Nanjirinji mpaka Ruangwa umekamilika, lini Serikali itajenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeshafanya kama alivyosema upembuzi yakinifu, na yote hayo ni maandalizi ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna mpango wa kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Kiranjeranje hadi Ruangwa kwa kadri fedha itakavyopatikana.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Naomba kumuuliza Naibu Waziri; barabara itokayo Masumbwe – Lugunga kuelekea Geita, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye mpango wa RICE, na sasa hivi kinachoandaliwa ni document tender kwa ajili ya kuitangaza ili barabara hii iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami kwa maeneo ambayo yameainishwa. Ahsante.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Bungu – Nyamisati imekuwa kilio cha muda mrefu sana kwa wananchi wa Jimbo la Kibiti; je, ni lini Serikali mtaitengeneza barabara hii katika kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Twaha Mpembenwe, Mbunge wa Kibiti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tayari tumeshakamilisha usanifu wa kina na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili tuweze kuijenga barabara hii yote kwa kiwango cha lami kuanzia Bungu mpaka Nyamisati. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, na pia namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali imekwisha kutenga fedha kwa mwaka wa fedha 2022/2023, je, ni lini Serikali itatoa hizo fedha ili ujenzi wa barabara uendelee?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa mkandarasi amekwisha kupatikana, na Naibu Waziri amesema kwamba Septemba ile kazi itakabidhiwa. Je, kwa kuwa mkandarasi amepatikana, ni lini ataanza hiyo kazi ili Septemba aikabidhi?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mkandarasi akishakabidhiwa anachofanya ni maandalizi ya ujenzi, na kwa hiyo kwa kuwa tumeshamkabidhi, na tumekubaliana lini atamaliza kazi, mkandarasi yuko site kwa maana ya kufanya maandalizi, na mwezi Septemba tunategemea atakuwa amekamilisha hiyo kazi, na kadri Serikali itakavyoendelea kupata fedha, barabara hii tuna uhakika itakamilishwa yote, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, ni lini Serikali itajenga barabara kwa kiwango cha lami kuanzia Kazegunga – Mahembe – Kitanga – Kinazi mpaka Buhigwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja ya Mahembe – Buhigwe – Kitanga ni barabara ya mkoa ambayo tayari tumeshakamilisha kufanya usanifu na sasa tunaendelea kumlipa huyo consultant na baada ya hapo tutaanza kufanya maandalizi kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, natambua kwamba ujenzi wa barabara ya Kisorya – Nyamswa – Bunda tayari umeshafika Nyamswa, lakini bado ujenzi unatakiwa uendelee na imekomea pale Makongoro Sekondari na inatakiwa ifike mpaka Isenye. Je, ni lini sasa ujenzi huo utaendelea kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ukishafika Nyamswa unapita kwenye T, aidha uende Mjini Musoma ama uende upande wa Nata. Na upande wa Nata ndiyo Isenye ambapo tayari kuna mkandarasi ambaye ameshajenga kutoka Makutano – Sanzate na Sanzate kwenda Nata tayari mkandarasi yuko site, nadhani kuna eneo Isenye pale tayari wameshajenga. Na wiki kama tatu nimekuwepo pale wakiwa wanaomba baada ya kuinua tuta wanahitaji kurekebisha maji pale, tumeshawarekebishia. Kwa hiyo, hiyo barabara iko kwenye ujenzi na mkandarasi yuko site (kilometa 40).

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara ya Mbuguni inayounganisha Mikoa ya Arusha na Manyara kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ilishaahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami, na tayari tumeshakamilisha usanifu. Sasa hivi Serikali inaendelea kuweka mipango ili tuweze kuijenga kwa kiwango cha lami. Naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira tuangalie kwenye bajeti tunayokwenda kuileta mbele yenu, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara hiyo ndiyo inaelekea Makao Makuu ya Halmashauri. Kwa kujenga kilometa mbili kwa mwaka barabara ya kilometa 79; je, Serikali ina mkakati gani wa makusudi kabisa wa kuimaliza barabara hii kwa wakati kwa kuzingatia umuhimu wake? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili. Nataka Serikali inieleze kwa dhati ya moyo kabisa, inamaliza lini Barabara ya kutoka Mtwara Mjini kupita Tandahimba – Newala mpaka Masasi ile ya kilometa 210? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, Mtwara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii kweli ni ndefu na inaenda kwenye Makao Makuu ya Wilaya. Ndiyo maana tumeshaifanyia usanifu, lakini kadiri fedha inavyopatikana tumeona tuanze kuijenga wakati tunatafuta fedha ya kuijenga yote kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, dhamira ipo ndiyo maana tumeanza.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, barabara ya kilometa 210 ya kutoka Mtwara – Mnivata – Newala hadi Masasi, Serikali imeshaanza kuijenga; kilometa 50 kutoka Mtwara hadi Mnivata, na sasa hivi tuko kwenye maandalizi ya kuanza kuijenga barabara yote kuanzia Mnivata hadi Masasi. Tumegawa lots mbili, kwa wahisani ya wenzetu wa African Development Bank ambao wanafadhili hiyo barabara, ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Je, ni lini Serikali itatenga fedha za kutosha kwa ajili ya kujenga barabara ya Ramadhani – Iyai, Mkoani Njombe ambayo iko kwenye Ilani ya CCM kwa zaidi ya miaka 15?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii barabara ya Ramadhani
– Iyai tumeshaanza kuijenga kwa awamu. Mwaka huu nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeitengea pia fedha kwa ajili ya kuendelea kuijenga. Matazamio ya Serikali ni kuikamilisha barabara yote hii kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa barabara ya Kakonko – Kinonko – Guarama mpaka mpaka wa Muhange, ambayo ni barabara itakayounganisha Tanzania na Gitega, ambayo ni Makao Makuu mpya ya Burundi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge Viti Maalum, Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kuanzia Kakonko hadi Muhange ni kweli inaunganisha Tanzania na Burundi na sasa hivi Makao Makuu yao yamesogea Gitega. Ilikuwa haijafanyiwa usanifu, lakini tutakamilisha usanifu ikiwa ni maandalizi kwa kuijenga barabara hii yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Kibaoni – Majimoto – Inyonga?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, Katavi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ilishatolewa ahadi na ipo kwenye Ilani. Naomba Mheshimiwa Mbunge awe na Subira, tuone bajeti tutakayopitisha, naamini kuna mapendekezo ya kuanza kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami, kuunganisha Mkoa wa Katavi na Mkoa wa Tabora, ahsante.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Karera – Munzeze – Janda hadi Buhigwe, kilometa 72 kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Karera – Muzenze hadi Buhigwe tayari ipo kwenye kukamilishwa kufanyiwa usanifu barabara yote ikiwa ni maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami. Tayari ipo kwenye usanifu na tupo kwenye hatua za mwisho, ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Lyazumbi inayounganisha Mkoa wa Rukwa na Katavi kupitia Mbuga ya Wanyama Katavi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hii ni barabara kuu, lakini kabla ya kuijenga hiyo barabara, ndiyo maana tumeamua kuijenga kwanza barabara ya Kizi – Kibaoni, Kibaoni kwenda Stalike. Kwa sababu hizo barabara zitakuwa zinakwenda parallel, baada ya kukamilisha, ndiyo sasa tutahamia pia kwenye hiyo barabara ambayo inapita katikati ya mbuga, ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya lami kutoka Airport kwenda Nyanguge yenye kilometa 47? Kwa sababu, upembuzi yakinifu umeshafanyika na barabara hii ni Bypass ya kupita Serengeti?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Matondo, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mwanza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni moja ya barabara ya Bypass katika Mkoa wa Mwanza, Airport – Igombe – Kayenze hadi Nyanguge. Namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na Subira, tuone bajeti hii tutakuwa tumepanga nini? Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujua kwenye mwaka uliopita, katika bajeti Naibu Waziri, aliahidi kujenga barabara ya Bariri – Mgeta; je, sasa iko kwenye bajeti inayokuja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, barabara hii amekuwa anaifuatilia; na kwa kuwa bado hatujapitisha bajeti, naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira tuone kama hii barabara tumeshaipangia bajeti. Mpango wa Serikali ni kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini barabara ya kilometa tano ya kutoka Kinyanambo C – Mapanda mpaka Kisusa, Jimbo la Mufindi Kaskazini, itajengwa? Kwa sababu hii barabara inafungua uchumi wa Mufindi Kaskazini.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati, Mbunge Viti Maalum, Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii aliyoitaja ni kweli inafungua uchumi, lakini ujenzi wake pia utategemea na upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kadiri fedha zitakavyokuwa zinapatikana, barabara hii itajengwa yote kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, barabara inayoanzia Wilaya ya Rorya inapita Susuni – Sirari – Mbogi – Nyansincha mpaka Nyanungu ni barabara ya kiusalama ambayo iko mpakani.

Nilitaka kujua barabara hii ni lini itajengwa kwa kiwango cha lami ili kuweza kuimarisha usalama katika mpaka wa Tanzania na Kenya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri barabara hii kabla ya kuja Bungeni nimeipitia yote, na ikiwa ina mahitaji makubwa sana pia ya Mkoa wa Mara kwa maana ya usalama. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaifanyia kazi kuhakikisha kwamba hii barabara inaimarishwa na kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Manispaa ya Singida ipo katikati ya nchi na malori kutoka upande wa nchi yanapita pale; je, Serikali haioni kwamba kuna umuhimu wa kuwahisha ujenzi wa bypass hii ili kuondoa msongamano unaokua kwa kasi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Wakati wenzetu wanaongelea Bypass, Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama haina hata mita moja ya lami; na kwa kuwa, upembuzi yakinifu wa barabara ya Simiyu – Singida umekamilika: Serikali haioni haja katika bajeti hii kutenga walau kilometa 20 Makao Makuu ya Halmashauri ya Mkalama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Mtinga, Mbunge wa Mkalama, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Singida kuna traffic kubwa. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba tumekamilisha mwaka 2022 kufanya usanifu na tunavyoongea sasa hivi, tayari tumeshafanya tathmini ya wale watakaofidiwa kupisha barabara; na Serikali inaandaa malipo kwa ajili ya kuwafidia hawa watu watakaopisha barabara. Kwa hiyo, tunataka tumhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Singida kwamba, Serikali imedhamiria kwa dhati kujenga hiyo bypass.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunatambua kwamba barabara aliyoitaja ni muhimu sana ambayo pia ni kutoka Singida kwenda Sibiti hadi Bariadi. Naomba pia, avute Subira, tuone kwenye bajeti hii inayokuja tumetenga nini? Ahsante.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nyaraka za kiofisi tulizonazo kutoka Serikalini zilionesha kwamba katika barabara hii, usananifu na upembuzi yakinifu ungekamilika mwezi wa Sita lakini sasa tunaambiwa ni mwezi wa Tisa: Je, Waziri anaweza kuniambia mpaka sasa kazi iliyofanyika, imefanyika kwa kiwango cha asilimia ngapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kutokana na umuhimu wa barabara hii kiusalama na kiuchumi, Wizara ipo tayari kutenga fedha ili ujenzi uweze kufanyika kwenye lots ambazo kazi imeshakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dunstan Luka Kitandula, Mbunge wa Mkinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu asilimia ambayo imefikiwa, naomba baada ya kikao hiki niweze kupata taarifa kamili kwa sasa tuko asilimia ngapi? Hata hivyo nataka tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pengine kitu muhimu hapa ni lini tutakamilisha hii kazi ambayo kwenye jibu langu la msingi nimesema kazi hii ya usanifu itakamilika mwezi Septemba. Kwa maana ya takwimu, asilimu naomba nitamjulisha Mheshimiwa Mbunge mara baada ya kutoka hapa kupata taarifa kamili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba barabara hii ni muhimu sana kiusalama na kiuchumi na ndiyo maana tumeamua kuifanyia usanifu wa kina ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kwa niaba ya wananchi wa Makete nipende kuishukuru Serikali kwa kuichukua barabara hii ya kutoka Chimala kuelekea Matamba kilomita 20 ambayo ina kona 53 kwenye milima. Barabara hii ni ya kiuchumi na barabara ya kimkakati, kwenda TANROADS ni msaada mkubwa ambao Serikali imeweza kutusaidia.

Je, kwa kipindi hiki ambacho mvua nyingi zinaendelea Matamba na Makete ni upi mpango wa Serikali kutusaidia barabara hii iweze kupitika kwa sababu wananchi wanaitumia sana kwa muda mwingi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kuna barabara kutoka Kitulo kuelekea Busokelo kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Uchukuzi, upi mkakati wa Serikali kuimalizia barabara hii ili iweze kujengwa irahisishe mawasiliano kati ya wananchi wa Makete na wananchi wa Jimbo la Busokelo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Matamba hadi Kitulo ni eneo ambalo kwa kweli Mheshimiwa Mbunge atakubaliana na mimi lina mvua nyingi sana, na TANROADS wako barabarani kuhakikisha kwamba inapitika lakini yako maeneo ambayo tunashindwa kufanya kazi kwa sababu ya mvua nyingi sana ambayo inaendelea kunyesha. Hivi tumewaagiza TANROADS kuhakikisha kwamba muda mwingi wawepo maeneo hayo ili pale ambapo jua linatoka basi waweze kuhakikisha kwamba wananchi wanapata mawasilano na kurekebisha zile barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kwa swali lake la pili, kuhusu kutengeneza barabara ya Kitulo kwenda Busokelo; hii barabara haikuwepo, ni mpya. Atakubaliana nami kwamba tumeshaanza kuifungua na tumeifungua yote, kinachosubiriwa sasa ni kuikamilisha, kwa maana ya kujenga makalavati na kuweka changarawe ili kuhakikisha kwamba wananchi wa pande hizi mbili wanaweza kuwasiliana, na hasa wananchi wa Busokelo kwenda Hospitali ya Ikonda ambao wanaihitaji sana, ahsante.
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru: -

Je, ni lini Serikali itafanya upembuzi yakinifu kwa barabara ya Mwembe-Mbaga na hatimaye kuijenga kwa kiwango cha lami kwa sababu imekuwa ni changamoto kubwa sana kwa wakazi wa milimani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mbunge awe na Subira, barabara nyingi sana tunategemea kuzifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Tukiwa tunajua tunaelekea mwisho wa utekelezaji wa ilani ya chama, kwa hiyo tunaamini barabara zote ambazo zimeainishwa kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina tutazifanya kuanzia mwaka huu na mwaka ujao wa fedha, ikiwepo na barabara ya Mheshimiwa Mbunge aliyoisema, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante; Barabara ya Mpunze-sabasabini ipo Nyagholo mpaka Igwamanoni imekatikakatika haipitiki kabisa na imepandishwa kutoka TARURA kwenda TANROADS. Ni nini mkakati wa Serikali kwa ajili ya kuijenga barabara hii angalau hata kujua maeneo yaliyokatika ili wananchi waweze kupita kwa urahisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cherehani, Mbunge wa Ushetu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara aliyoitaja ilikuwa inahudumiwa na wenzetu wa TARURA, na ndiyo kwanza imekuja sasa TANROADS. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa wa Ushetu pamoja na wananchi wa Ushetu, kwamba tumesikia, na ninamwagiza Meneja wa Mkoa wa Shinyanga, cha kwanza aende akahakikishe kwamba yale maeneo yote ambayo yamekatika anayarejesha ili kuwe na mawasiliano. Pia aweze kufanya tathmini ili maeneo yote yale korofi tuweze kuangalia namna ya kuyarakabati vizuri ili yaweze kupitika muda wote hata kipindi cha masika, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Mafinga Mgololo inapita katika majimbo matatu, kwa maana ya Mafinga Mjini, Mufindi Kaskazini na Mufindi Kusini. Katika majibu ya Serikali mara zote wanasema kwamba barabara hii iko chini ya utaratibu wa EPC+F, na kwamba Wizara ya Ujenzi wao wameshamaliza kazi suala hili liko hazina. Sasa wananchi wa Wilaya ya Mufindi wanatuuliza sisi Wabunge wao watatu, kwamba;

Je, hawa wa ujenzi hawawezi kwenda huko fedha kuwaambia sasa watoe fedha hii barabara ianzwe kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimwakikishie Mheshimiwa Chumi, Mheshimiwa Kihenzile na Mheshimiwa Kigahe, kwamba barabara aliyoitaja ya hawa Wabunge wote ipo na hakuna barabara ambayo imeachwa katika huu mpango wa EPC+F. Kwa kweli taratibu zinakwenda vizuri tupo tunakamilisha taratibu na nadhani kipindi cha bajeti hizi barabara zote nategemea tutaziwakilisha na zianze utekelezaji, ikiwepo na barabara ya Mgololo hadi Mafinga, ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Sera ya Taifa letu ni kuunganisha barabara za mikoa kwa lami, lakini sisi Mkoa wa Lindi haujaunganishwa na Mkoa wa Morogoro kwa barabara hata ya vumbi.

Je, Serikali inasema nini juu ya kuunganisha sisi Mkoa wa Morogoro na Lindi kwa barabara angalau ya changarawe pale Liwale na Mahenge?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge Kuchauka, kwamba mwaka huu wa bajeti tumependekeza kwanza tufanye upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kati ya Liwale, Ilonga hadi Mahenge ili hii barabara tuweze kuifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara inapita kwenye Mbuga ya Selous, na limekuwa ni ombi kubwa sana la wanalindi akiwepo Mheshimiwa Kuchauka sasa tumeiweka kwenye mpango wa kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa hiyo kama bajeti yetu itapita tuna uhakika hiyo kazi itakuwa imeanza kuunganisha Mkoa wa Lindi na Mkoa wa Morogoro, ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami Barabara ya Mwanango kupita Kahama inayounganisha Mkoa wa Shinyanga ili kukuza uchumi na ipo kwenye ilani ya uchaguzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Matondo, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Mwanza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii tulishakamilisha usanifu wa kina na tumeanza kuijenga kwa hatua na hasa maeneo ambayo ni ya mijini, ikiwa ni mpango wa Serikali kutafuta fedha kuijenga barabara ya Mwanangwa-Solwa hadi Kahama kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru majibu mazuri ya Serikali, lakini kwa kuwa kukosekana kwa hicho kivuko kumekuwa kunatokea ajali za mara kwa mara. Kwanza kwa wananchi vilevile kwa bajaji pamoja na magari. Sasa nilitaka nifahamu kwamba kwa nini Serikali isione kwamba kuna umuhimu mkubwa sana wa kuharakisha upatikanaji wa hizo fedha ili hicho kivuko kiweze kujengwa ili kuwapunguzia adha kubwa wanayopata wananchi wa Mji wa Tunduma; vilevile ikizingatiwa kwamba ilikuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo analolisema na changamoto anayoisema mimi binafsi ninaifahamu na ni sehemu ambayo na mimi barabara hii naitumia sana. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba jitihada zimeshaanza kuchukuliwa kuweka hizo alama za kusaidia kupunguza ajali.

Mpango wa Serikali kwa sasa tayari wanafanya usanifu kuangalia namna ya kuweka kivuko cha chini badala ya kivuko cha juu kwa sababu tumekuja kuona kwamba mara nyingi vivuko vya juu havitumiki sana kuliko vivuko vya chini.

Kwa hiyo nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge, Serikali inatambua na iko tayari kuwalinda wananchi na kivuko hicho kitajengwa kama kilivyoahidiwa na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, natoa pole kwa wananchi wetu wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara kwa mafuriko makubwa ambayo wameyapata, na tunashukuru Mungu mpaka sasa hakuna kifo kilichotokea, tunapambana kupeleka misaada kwa wananchi ambao wameathirika sana. Mafuriko haya yamethibitisha kwamba kuna miundombinu ya TANROADS katika Kalavati la Sheli ya Madinga kwenda Rumomo na Kalavati la Kwa Shungu kwamba ni madogo na ndio yalichangia kupatikana kwa mafuriko.

Je, Serikali ina hatua gani za haraka za kurekebisha makalavati haya kama tulivyotembea na Mheshimiwa wa Wilaya na kujionea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba nitumie nafasi hii kumwagiza Meneja wa Mkoa wa Morogoro aende hilo eneo ambalo makalavati ni madogo atafute namna ambavyo anaweza akaongeza hayo makalavati kwa haraka ili kuondoa changamoto ambayo inawakuta wananchi wa Jimbo la Kilombero kwa Mheshimiwa Asenga, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Spika, naomba nimuulize Naibu Waziri maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa mwaka wa fedha 2023/2024 umebaki miezi miwili.

Je, ni lini wananchi wa Kigamboni watarajie vivuko hivyo viwili vidogo kama Mheshimiwa Naibu Waziri anavyoongea?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa kuwa TEMESA ni Taasisi ya Umma inayotoa huduma za ufundi na umeme pamoja na huduma za vivuko.

Je, Serikali haioni sasa umefika muda muafaka wa kushirikisha sekta binafsi katika kutoa huduma ya vivuko ili kuongeza ufanisi na kuongeza wigo wa huduma hususani kwa wananchi wa Kigamboni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, mwaka huu tulitegemea tuanze manunuzi ama utengenezaji wa kivuko na kazi hiyo tumeshaanza, kwa sababu tulitangaza tenda kununua hivi vivuko viwili lakini ilionekana watu hawa walikuwa wame-bid, wote walikuwa wame-tender bei za juu wakati wa kufanya evaluation, hivyo tunatangaza upya tena tenda, kwa hivyo tupo kwenye utekelezaji wa bajeti ya mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kigamboni na Magogoni kwamba hizo taratibu zinaendelea tutakapopata Mkandarasi sahihi shughuli hizo zitaanza mwaka huu wa fedha na tayari tumeshaanza.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, tayari yalikuwa pia ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwamba taasisi zote ambazo zinafanya biashara kama kuna uwezekano wa watu binafsi kufanya biashara basi waruhusiwe, hivi ninavyoongea tayari Azam ameshaonesha nia ya kutaka kufanya shughuli katika kivuko hiki cha Kigamboni na sasa itakuwa ni kwa vivuko vyote tunategemea Serikali ikishakamilisha taratibu basi wale wafanyabiashara ambao wanataka kufanya biashara sambamba na TEMESA taratibu zikishakamilika wataruhusiwa kufanya hivyo. Ahsante.(Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Ninataka nijue tu ni lini Serikali itarejesha kituo cha MV Musoma kilichokuwa kinatoa huduma kati ya Kinesi kwa maana ya Rorya na Musoma Mjini hasa ukizingatia kituo kilichopo ni kidogo na hakikidhi mahitaji ya watu lakini pia ni hatari kwa maisha ya wananchi wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kivuko cha Musoma - Kinesi kiliazimwa kwenda kufanya kazi kati ya Kisolya na Lujezi, Musoma tulipeleka kivuko cha Chato One. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunategemea mwishoni mwa mwezi huu Tarehe 30 Kivuko cha Kisolya- Lugeza ambacho kilikuwa kinatengenezwa kitakamilika na mwanzoni mwa mwezi unaokuja kivuko cha MV Musoma kitarudishwa kwa ajili ya kutoa huduma iliyokuwa imezoeleka kati ya Musoma na Kinesi. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, kwenye mradi wa SGR kwenye eneo la Kikongo pamoja na Msuwa kuna uhitaji wa kuweka kivuko na TRC waliahidi kuweka ni muda mrefu sasa.

Je, Waziri atakuwa yuko tayari kutoa agizo kwa Mkururgenzi wa TRC kukamilisha mradi huo kabla haujaanza utekelezaji wake?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakamo Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumejadili na Mheshimiwa Mbunge na tayari nilishatoa maelekezo kwa Mtendaji wa TRC ili waweze kuangalia eneo hilo ambalo ni muhimu sana kuwa na kivuko kwa waenda kwa miguu ili waweze kuangalia uwezekano wa kujenga kivuko mahali aliposema Mheshimiwa Mbunge, ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Gati la kushukia abiria jengo la mizigo ya wasafiri, jengo la abiria Bandari ya Manda Wilayani Ludewa utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Gati la Manda upo kwenye mpango, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutahakikisha kwamba tunajenga gati hili la Manda ili wananchi wasipate changamoto ambayo wanaipata sasa hivi, ahsante.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa pesa nyingi sana kwa ajili ya ujenzi wa kivuko cha Mwaya – Kajunjumele; je, ni sababu gani zinafanya mpaka sasa hivi kisianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kati ya Mwaya- Kajunjumele tuna kivuko ambacho kilitoka Luhuhu kiko site na tunachosubiri sasa hivi ni kwamba maji yaweze kupungua ili tuweze kurekebisha rampu halafu baada ya hapo kivuko hicho kitaanza kutoa huduma kati ya Mwaya na Kajunjumele, ahsante.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Katika Jimbo la Singida Kaskazini Kijiji cha Kinyeto na Ilongero kuna bwawa la Ntambuko ambalo wananchi wanapata shida...

SPIKA: Swali lako.

MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali italeta kivuko katika bwawa la Ntambuko linalounganisha Kijiji cha Itamuka, Ilongero na Kinyeto?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba tumelichukua hilo na TEMESA watakwenda kufanya study ili waone kama kivuko kinaweza kikajengwa kwenye hilo bwawa alilolisema kwa ajili ya kurahisisha mawasiliano kati ya wananchi wa pande hizo mbili. (Makofi)
MHE. BENAYA L KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri ambayo yanatia moyo wananchi hawa wa Wilaya ya Mbinga kwa maana ya barabara hii ya Litembo ambayo imesubiriwa kwa muda mrefu na inaahadi za Marais Watatu kujengwa kwa kiwango cha lami, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Matiri kwa maana ya Kigonsera hadi Matiri ambako kuna kilimo kikubwa cha maharage na mahindi inapitika kwa shida sana, sasa wakati tunasubiri mchakato huo kuendelea, Serikali inampango gani wa kuifanya hii barabara iweze kupitika kwa msimu mzima?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara ya kutoka Liyombo kuja hadi Rwanda kupitia Mdunduwalo ambayo Makaa ya Mawe yanapita hivi sasa ama haipitiki baadhi ya siku, ama inapitika kwa shida sana, tumeleta maombi maalum ni lini sasa Serikali itaitengeneza barabara hii kupitisha makaa ya mawe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Matiri - Kigonsera kama alivyoisema kweli ni barabara ya changarawe ambapo sasa hivi ni kipindi kikubwa ambacho mvua kubwa sana inanyeesha naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshatoa taarifa kwa mameneja wote wa TANROADS Tanzania kuhakikisha kwamba barabara zote ambazo zinachangamoto waweze kuzisimamia kwa ukaribu na narudia tena kumsisitiza Meneja wa Mkoa wa Ruvuma ahakikishe kwamba barabara ya Matiri – Kigonsera inapitika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala lake la pili la kutoka Liyombo hadi Rwanda hii ndiyo barabara ambayo inasafirisha sana Makaa ya Mawe na kuna migodi kama minne, ambayo pia Mheshimiwa Waziri Mkuu alitoa maelekezo tuweze kuitengeneza.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii tutahakikisha kwamba inapitika na kama nilivyosema kwamba kwenye barabara zingine Mkandarasi yuko site kwenye hayo maeneo lakini inategemia na hali ya hewa. Kwa hiyo, Mkandarasi yuko site kuhakikisha kwamba patakapotokea nafuu ya hali ya hewa wataendelea kuitengeneza hiyo barabara ili iweze kupitika. Ahsante. (Makofi)
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kufahamu ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kutujengea barabara ya Mlowo – Kamsamba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, babrabara ya Mlowo - Kamsamba naomba Mheshimiwa Mbunge avute subira ni barabara ambayo imepigiwa sana kelele katika Bunge hili, kwa hiyo tunategemea kwamba itakuwa kwenye mapendekezo kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. NORAH W. MZERU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati barabara ya Isimilo - Kilombero ili kuwasaidia wakulima kupitisha mazao yao kwa urahisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii naamini inatengenezwa na inakarabatiwa, changamoto kubwa ambayo tunayo sasa hivi ni barabara nyingi katika kipindi hiki cha mvua kunatokea changamoto, pia nitoe tu maelekezo tena kwa Meneja wa Singida kuhakikisha kwamba anaisimamia hii barabara na inapitika muda wote wakati huu wa kilimo kwa wananchi, ahsante.
MHE. DKT. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara ya Makambako - Songea hasa eneo la Madaba kuanzia Igewisinga mpaka Mtiangimbole limebomoka vibaya sana kiasi cha kuhatarisha usalama wa watumiaji. Je, ni lini sasa Serikali itaijenga hii barabara kwa uhakika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nimemuelewa vizuri hii ni barabara kubwa ya kutoka Makambako kwenda Songea, hii barabara ipo kwenye mpango wa kukarabatiwa na World Bank, sasa hivi tutaanzia Lutukila kwenda Songea ikiwa ni pamoja na bypass ya Songea Mjini, wakati huo sasa inatafutwa fedha kuanzia Makambako hadi Lutukila.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona.

Kwa kuwa, Serikali imeshatoa Milioni 300 kwa ajili ya upembuzi wa barabara ya kutoka Kahama - Nyang’wale – Busolwa - Busisi - Sengerema kwa kiwango cha lami, na huwa unanijibu majibu ya kisiasa nataka leo unijbu, ni lini upembuzi huo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tukishatenga fedha kwenye bajeti nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita iko makini, ikishatenga maana yake tunatekeleza, isipokuwa tu ni hatua kuwa hatua ndefu.

Mheshimiwa Spika, barabara inayotwa siyo barabara fupi Kahama Nyang’wale - Ngoma hadi Busisi ni parefu, kwa hiyo iko tayari inafanyiwa kazi nakuhakikishia baada ya kukamilika ndiyo sasa tutajua gharama ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, ahsante; je, ni lini barabara ya Bariadi – Ngulyati kwenda Magu itajengwa kwa kiwango cha lami kama ilivyoainishwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sabu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, pia hii barabara ni kati ya barabara ambazo zimeongelewa sana. Namwomba Mheshimiwa Mbunge tusubiri, tutakapoleta bajeti yetu watupitishie, na ninaamini itakuwa ni moja ya barabara ambazo zitakuwepo kwenye mpango, ahsante.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Barabara ya Iringa – MR – Itunundu iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi zaidi ya miaka 30. Ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge, kwanza itatakiwa iingizwe kwenye usanifu wa kina, baada ya hapo tukishafanya hiyo kazi, ndiyo tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, tunatambua kwamba iko kwenye Ilani, ifanyiwe usanifu na ninaamini kazi hiyo tutaifanya katika kipindi hiki cha miaka mitano, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Barabara ya kutoka Hoteli Tatu – Pande – Lihimalyao iko chini ya TARURA, lakini Bodi ya Barabara pamoja na Kamati ya Ushauri ya Mkoa wa Lindi ilipendekeza barabara hii iapandishwe hadhi, ichukuliwe na TANROADS; ni lini TANROADS itaichukua barabara hii? (Kicheko)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge aweze kuleta swali mahususi, ahsante. (Makofi)
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kilometa 52 kutoka Kilindoni mpaka Rasi Mkumbi, Kisiwani Mafia ni lini zitakamilika kwa ujenzi wa lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyotaja Mheshimiwa Mbunge tumeitengea bajeti mwaka huu unaoendelea na tutaendelea kuitengea katika mwaka unaokuja hiyo barabara ambayo iko katika Kisiwa cha Mafia, ahsante. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Tumeshuhudia mvua kubwa zinazoendelea nchi nzima na kufanya mawasiliano katika baadhi ya maeneo kukatika na hivyo kuchukua muda mrefu kuzitengeneza kwa wakati ili wananchi waweze kuendelea na usafiri na usafirishaji, lakini kuokoa uhai wa watu kwa wale ambao labda wanahitaji huduma hizo kwenda hospitali na vinginevyo: -

Nini mkakati wa Serikali wa haraka endapo inatokea changamoto ya namna hiyo, inafanyika kwa haraka na mawasiliano yanarudi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Paresso, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunategemea tutaoa taarifa, kama alivyoongea hata juzi Mheshimiwa Kunambi. Barabara nyingi ambazo tunazo Tanzania, ni Kilometa kama 36,000 ambazo tunazihudumia. Kati ya hizo, ni kilometa 12,000 tu ambazo zina lami. Kwa hiyo, barabara hizi zenye urefu wa kilometa kama 24, nyingi ni za changarawe na nyingine zipo mabondeni ambazo tumeshatoa taarifa kwa wakuu wa barabara kwa maana ya Meneja wa TANROADS kuhakikisha kwamba barabara zote ambazo zinakuwa na changamoto wanazi-attend kwa muda.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambapo ni kwenye madaraja, tuna madaraja ya muda ya chuma ambayo kama ni daraja linaweza lakini bahati mbaya unakuta siyo tu daraja limeondoka, lakini ni tuta pengine la kilometa moja mpaka mbili limeondoka na wakati mvua inanyesha inakuwa ni ngumu kuweza kufanya hiyo kazi wakati pana maji, ahsante.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza nimshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri sana ambayo ameyatoa sasa hivi. Nilikuwa na kitu kwanza kidogo kabla sijampa maswali yangu ya nyongeza mawili niliyonayo.

Nashukuru kwamba mwezi wa Ramadhani wenzetu wa jamii, wenzetu humu Bungeni walituheshimisha sana, wote walikuwa wanavaa mashungi na wanaume walikuwa wakivaa kanzu pamoja na koti, hilo kwanza niwashukuru sana na Mwenyezi Mungu awajaalie wazidi kutufuata sisi wenzetu Waislam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina maswali mawili ya nyongeza, zipo nchi zimefanikiwa kujenga daraja za umbali mrefu, kwa nini tusipate uzoefu kutoka kwao?

Swali langu la pili, je, kwa nini usitumike mpango wa ubia na sekta binafsi PPP kwa ajili ya ujenzi huo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi, upande wa Zanzibar na upande wa Tanzania Bara, wahusika tayari wameshakutana kwamba hili suala linazungumzika na lipo linachakatwa, bado yatokanayo na hilo hayajapatikana ikiwa ni pamoja na kulifanyia kazi lile alilosema Mheshimiwa Mbunge kupata uzoefu kutoka sehemu mbalimbali ambazo wenzetu wameshajenga madaraja mengine marefu kama haya, ndiyo maana tunasema yatokanayo na hayo bado lakini suala hilo lipo linafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la pili kuhusu PPP, ni kweli kabisa kwamba siyo mpango kwa maana ya Serikali ichukue fedha zake ijenge na hata hao walioonesha nia ni sekta binafsi. Kwa hiyo, tunaamini daraja hili kama litajengwa, litajengwa kwa mtindo wa PPP kama alivyoshauri Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Denmark kuna daraja linalounganisha Odense na Sealand na lilichukua muda mfupi sana kujengwa.

Je, Serikali inatueleza nini katika kupeleka mtu kama mwenye swali lake Mwantumu Dau Haji kwenda kulishuhudia ili tufupishe hayo maneno ya mazungumzo yalifanyika, yalifanyika kwa muda mrefu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mazungumzo yalifanyika Mwezi Machi mwaka huu na huu ni mwezi Aprili. Kwa hiyo, kwa mradi mkubwa kama huu na daraja ambalo linaunganisha linategemewa liunganishe Bara na Zanzibar yako mambo mengi sana ambayo yatafanyika. Moja ya eneo ambalo tunafahamu ni Denmark lakini hata China wana madaraja mengi marefu. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla Serikali haijaanza kutekeleza lazima watajiridhisha kwa mambo mengi sana ikiwa ni pamoja na teknolojia mbalimbali ambazo zimetumika katika nchi nyingine ambazo wana madaraja marefu kama haya. Ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mzauri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa kuanza ukarabati wa majengo haya ila kwa kuwa yamekaa muda mrefu, nataka kufahamu kama mwaka huu wa fedha unaokuja fedha zimetengwa kwa ajili ya kumaliza ukarabati kwa ajili ya majengo yote yaliyobakia na ukarabati utategemea kumalizika kwa muda gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ni kwamba Serikali haioni umuhimu wa kujenga mradi kama ule wa Magomeni, Ukonga ili wananchi waweze kupata nyumba na majengo mengine waweze kukodiwa watumishi ikiwemo watumishi wa Magereza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge yote kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo ya Ukonga kota ni majengo yale madogo na ya zamani na mpango wa Serikali kama ilivyoelekezwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi maeneo yote ambayo yalikuwa na majengo yale ya zamani yaboreshwe ama yabadilishwe na Ukonga ikiwa ni moja ya eneo ambalo mwezi huu wataalam wamekwenda ku–assess na kupata ukubwa wa eneo halisi ili paweze kubadilishwa na kujenga majengo makubwa ya ghorofa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi mpango mzima ni kujenga majengo yanayokwenda juu badala ya kuejenga haya majengo madogo. Kwa hiyo, Ukonga kota ni sehemu mojawapo kama Temeke, Ilala kota, Kinondoni, Ghana Mwanza na hata Arusha. Kwa hiyo, maeneo yote haya tunafanya mabadiliko ya kujenga ghorofa kama ambavyo tumejenga Magomeni kota na tunavyoendelea Temeke, ahsante.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafsi ya kuuliza swali la nyongeza.

Manispaa ya Moshi tunazo Kata ambazo ziko katika maeneo ya Majengo Kiusa na kota hizo zimechoka sana na ni za miaka mingi sana. Wako wapangaji ambao wameishi pale mpaka sasa hivi wana wajukuu na vitukuu.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha kota hizo au hata kama kuna uwezekano wa kuweza kuwauzia? Aahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu ssali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu la pili kwenye majibu yangu ya nyongeza kwa Mheshimiwa Kapinga, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, awamu hii ya sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan; moja, ameshatoa maelekezo kwamba, pale ambapo mnaweza mkafanya na sekta binafsi, basi kuna haja ya kufanya hivyo. TBA kwa jinsi muundo wake ulivyokuwa, sasa hivi iko kwenye kubadilishwa ili iweze kufanya na private sector ili maeneo yote yale ambayo yalikuwa na quarters zilizochoka tuangalie uwezekano wa kuongea na wenzetu wa sekta binafsi ili kuharakisha kujenga majengo kwa ajili ya kutoa huduma kwa watumishi na viongozi wa Tanzania hii, ahsante. (Makofi)
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Kwa kuwa Serikali imekubali maombi ya wananchi na wakazi wa Magomeni Quarter, familia 644 kuwauzia nyumba hizo na kuwapunguzia bei ya ununuzi na vilevile kuwaongezea muda wa kulipa kutoka miaka 15 hadi 30. Swali langu: Je, Serikali iko tayari kupokea shukrani zangu za dhati pamoja na wananchi wa Magomeni Quarter kwa uamuzi wa Serikali kuwauzia nyumba hizo na kuboresha familia zao, kitendo ambacho kinaonekana ni kuboresha maisha ya wananchi wa Tanzania? Shukrani hizi zimwendee Mheshimiwa Rais na Mtendaji Mkuu wa TBA Bwana Kondoro. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani alizotoa Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, naomba nizipokee shukrani hizo ambapo ni kazi kubwa imefanyika, na kweli amejali wananchi waliokuwa wanaishi hapo, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza: -

Je, ni kwa kiasi gani Serikali imejiridhisha kuwa marekebisho hayo yamekidhi viwango?

Swali la pili; kwa kuwa barabara ya Kolandoto – Meatu mpaka Kateshi iko kwenye ilani, je, ni lini Serikali itaijenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imejiridhisha kwanza kwa kumsimamia zaidi mkandarasi na kuhakikisha kwamba kila hatua anayoifanya mhandisi mshauri pamoja na mkandarasi kupewa majukumu ya kuhakikisha kwamba anakwenda kufanya kazi kwa kiwango kinachotakiwa. Hata hivyo, atakapokuwa amekamilisha kazi hii itahakikiwa na wataalam kuhakikisha kwamba vigezo vyote vya barabara kwa maana ya jinsi ilivyosanifiwa ndivyo ilivyorekebishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili; barabara aliyoitaja ya kuanzia Kolandoto – Meatu kwenda Katesh ni sehemu ya barabara ndefu ambayo ipo kwenye mpango pia wa EPC+F. Ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mwezi mmoja sasa tangu nisimame hapa nikiuliza kuhusu Barabara ya Masasi – Nachingwea, na Mheshimiwa Naibu Waziri utakumbuka ulinijibu kwamba iko kwenye hatua za financing. Na niliuliza lini mchakato huo utakamilika, hatukuweza kupata majibu wakati ule. Sasa ninauliza tena: -

Ujenzi wa Barabara ya Nachingwea – Masasi ambao ulikuwa kwenye hatua ya financing; hatua hiyo itakamilika lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ya Masasi Nachingwea inakwenda mpaka Liwale. Kama nilivyosema, ni kati ya barabara saba ambazo ziko kwenye EPS+F; na taratibu za manunuzi kwa maana ya upande wa finance kwa wenzetu wa fedha bado zinaendelea zote kwa pamoja, kwa barabara zote saba. Kwa hiyo zitakapokuwa mchakato huu umekamilika tutamjulisha Mheshimiwa Mbunge.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri, barabara ya Kibaha – Morogoro -Dodoma kwenda mpaka Mwanza hamuoni kama imelemewa sasa hivi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Kibaha hadi Morogoro ipo kwenye PPP ambapo itajengwa kwa express way njia nne; na kutoka Morogoro kuja Dodoma hadi Mwanza ni kweli magari yameongezeka. Serikali ina mpango wa kuipanua hiyo barabara ili iweze kukidhi haja ikiwa ni pamoja na maeneo yote ya miinuko na maeneo ya ku-park kuweza kuipanua ili iweze kukidhi mahitaji ya sasa, ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujua sasa barabara ya kutoka Kokoto mpaka Kongowe ni lini upanuzi wake utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, na swali la pili, Je, ni lini sasa barabara ile ya kutoka Mbande Kisee mpaka Msongora ambayo imekuwa ni adha kwa wapiga kura wa Dar es Salaam ujenzi wake utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze na barabara ya pili Mbande kwenda Msongora kilomita hizo tatu ambazo zimebaki tunategemea zitaanza kutekelezwa katika bajeti hii tunayoanza kuikamilisha. Na barabara hii ya Kokoto kwenda Kongowe upanuzi wake, naomba Mheshimiwa Mbunge asubiri tuone kwenye bajeti tumependekeza tufanye nini. Tunajua tayari kuna changamoto kubwa tuweze kuitekeleza hii barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika jimbo la Manyoni Mashariki kuna Barabara ya kutoka Sorya kwenda Hika – Makulu – Londoni na Ikungi Singida.

Je, ni lini Serikali itaanza kufanya upembuzi na usanifu wa kina kwa ajili ya kuijenga katika kiwango cha lami ? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika,naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo tumeipendekeza ifanyiwe usanifu mwaka wa fedha tunaoanza kama bajeti yetu itapitishwa, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa barabara yetu ya Kitonga kumekuwa na ajali nyingi sana, na wiki iliyopita tu basi lilitumbukia pale, na ajali ikitokea magari yanakaa takriban siku nzima au siku mbili. Je, lini Serikali itaona sasa umuhimu wa kujenga barabara mbadala ya kutoka Mahenge kwenda Udekwa kupitia Utalisoli mpaka Ilula?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika,ni kweli lile eneo la Kitonga limekuwa na changamoto kubwa. Tayari Serikali ilishatoa maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Iringa wasaidiane na Meneja wa TARURA Mkoa wa Iringa kuangalia uwezekano wa kufanya by-pass ya Mlima Kitonga ili kunapotokea changamoto kuwe na uwezekano wa kuwa na njia mbadala, ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, je, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa barabara inayotoka Buza kwenda kuunganisha jimbo la Ukonga pamoja na Temeke?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kusaidiana na wenzetu wa TAMISEMI tutahakikisha kwamba hiyo barabara tunaijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika,nashukuru, Mkoa wa Mtwara una unganishwa ni Mkoa wa Lindi hadi Morogoro kwa kuanzia katika Wilaya ya Nanyumbu. Barabara hii iko ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Je, ni lini barbara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, na kwa kweli tumeongea naye. Hii barabara ni kweli ipo kwenye Ilani. Inapotoka Wilaya ya Nanyumbu kwenda Liwale inapita Selous ambapo inakwenda Ilonga kwenda Mahenge kuunganisha na Mkoa wa Morogoro. Tumeweka kwenye mapendekezo kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili kuunganisha Mkoa wa Mtwara, Lindi na Mkoa wa Morogoro kupitia eneo la Ilonga – Mahenge, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika,ahsante. Je, ni lini Barabara ya Uvinza – Maragarasi yenye kilometa 51 itamalizika kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Uvinza - Maragarasi ni barabara ambayo ipo kwenye ujenzi kwa msaada wa Abu Dhabi na Kuwat Fund, kilometa 51.3 Mkandarasi yuko site. Kinachokwamisha sasa hivi kutokwenda kasi ni kwa sababu ya Mvua nyingi inayonyesha; lakini Mkandarasi ameahidi kwamba atakamilisha kwa muda kulingana na jinsi tulivyokubaliana naye, ahsante.
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naoma kujua ni lini Serikali itaona umuhimu wa kujenga barabara ya kutoka Chapwa halmashauri ya Mji wa Tunduma kuelekea Chindi mpaka Chitete ili kurahisisha mawasiliano ndani ya Wilaya ya Momba?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kwa sasa inahudumiwa na wenzetu wa TARURA, ambayo inaunganisha Makoa Makuu ya Wilaya ya Momba Chitete kuja Tunduma. Hata hivyo nitaichukua ili kama Serikali tuone namna tukavyofanya kuijenga kwa kiwango cha lami ili kuiunganisha Tunduma na Makao Makuu ya Wilaya ya Momba Chitete, ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nishukuru kwa majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa kituo cha Bukimwi kinachopokea abiria kutoka Kayenze nacho vile vile hakina Banda kwa ajili ya abiria kusubiri usafiri. Je, ni sehemu ya vituo vitakavyofanyiwa ujenzi kama ilivyo Bugorola, Kisorya na Ukara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Kivuko cha kutoka Kitale kwenda Ilugwa na kingine kutoka Kakukuru kwenda Ghana ni vivuko vilivyoko kwenye maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi mwaka 2020 - 2025. Je, Serikali ina mpango gani kuanza ujenzi wa vivuko hivi kwa ajili ya kuokoa maisha ya wananchi kwenye eneo hilo? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kwa awamu. Nikiri hivi vivuko alivyovisema viko kwenye ilani, lakini katika Ziwa Victoria tunajenga vivuko vipya vinne na katika Vituo vya Bukimwi – Kayenze vituo hivi kwa sasa haviko kwenye mpango wa kuvijenga kwa mwaka huu wa fedha labda kwa mwaka wa fedha unaokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vituo alivyovitaja vya Kitale – Ilugwa, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafahamu na tuna uhakika kadri idadi ya watu inavyoongezeka kuna haja kubwa sana ya kuongeza vituo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa visiwa hivi kwamba Serikali inafahamu na tunalifanyia kazi kutafuta fedha kuhakikisha kwamba tunakuwa na mawasiliano katika vile vivuko alivyovitaja vya Kitale, Ilugwa hadi Ghana, ahsante sana.
MHE. DKT. TEYA M. NTARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Katika Daraja la Kijazi ile flyover ukipita inavutia na imenyooka, sasa ukiendelea kule mbele ukapita kwenye ile flyover pale VETA yaani sisi tunaoangalia inaonekana pale juu ukingo ule umepinda. Mheshimiwa Waziri, anasemaje kuhusu ile? Inaleta picha mbaya.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kama Serikali tuchukue na tuliangalie kama limepinda ama ni design, halafu tutakuja kulitolea majawabu kama tatizo lilikuwa ni usanifu ama tatizo lilikuwa ni Mkandarasi kama anachosema Mheshimiwa Mbunge kitaonekana kwamba kina mapungufu, ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Mbeya ni jiji lakini hatuna stendi kubwa ya kutosha, stendi ile ni ndogo lakini hata taa haina. Je, ni lini Serikali itajenga stendi kubwa ya kutosha kwenye Mkoa wetu wa Mbeya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu tulichukue kama Serikali na tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ambao hasa kwa kweli ndio wanaohusika na kujenga stendi hizi kwenye miji na majiji na kama TANROADS tutahitaji kusaidia, basi tutafanya hivyo ili Mkoa wa Mbeya hasa Jiji la Mbeya liweze kupata stendi kama alivyoomba Mheshimiwa Mbunge, ahsante.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kutoa masikitiko yangu kwa Serikali, majibu yaliyotolewa na Serikali kiukweli hayaridhishi. Kama Serikali yenye wajibu wa kutoa mwongozo kuhusu namna gani taa za barabarani ziwekwe haijatoa mwongozo mpaka sasa, hali hii inasababisha mamlaka zilizokasimiwa kufanya shughuli hii kuweka taa za barabarani kwa utaratibu wanaotaka wao. Kwa sasa hivi ukiangalia maeneo mengi taa zilizowekwa barabarani ni hafifu mno, hazina ubora, lakini bado taa hizo hizo zilizowekwa barabarani zimewekwa aidha upande mmoja hali ya kwamba ikitokea labda zimeungua eneo hilo linabaki giza. Hata hivyo, taa hizo hizo hazifanyiwi maintenance kwa muda unaotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; je, Serikali iko tayari sasa kama yenye mamlaka kutoa waraka au mwongozo ili mamlaka zilizokasimiwa ziweze kuleta maana halisi ya uwekaji wa taa barabarani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Jimbo langu la Ulyankulu tangu kuundwa kwake halijawahi kuwa na barabara ya lami hata kilomita moja. Hata hivyo, kwa sasa kuna ujenzi wa kilomita moja na nusu ambao unatekelezwa kama ahadi ya Mheshimiwa Rais Hayati Dkt. John Pombe Magufuli. Je, Serikali iko tayari kwanza kumalizia kilomita moja na nusu ya lami iliyobakia na kuweka taa za barabarani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rehema Juma Migila, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TEMESA ndiyo ambao wamepewa kazi ya kuweka na kusimamia taa za barabarani. Pia TEMESA ndio wataalam wa kufanya kazi hizo kwa upande wa Serikali. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pia kwamba taa kulingana na teknolojia inavyobadilika unaweza ukasema utaweka taa hizi lakini kadri teknolojia inavyobadilika taa zimeendelea kubadilika. Zamani tulikuwa tunatumia umeme sasa hivi tunatumia solar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama unaweza ukaweka Mwongozo unaweza pia ukawa unashindwa kwenda na teknolojia. Ndiyo maana katika jibu langu la Msingi nimesema wanakwenda kulingana na mabadiliko ya teknolojia na nini wenzetu duniani wanachofanya na wataalam ndicho wanachokifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwamba pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna aina mbili ya barabara na tuna taasisi mbili zinazosimamia barabara. Katika Mkoa wa Tabora ambao Mheshimiwa Mbunge anatoka, katika mtandao wa taa mkoa mzima tuna taa 1,568 mpaka leo ninavyoongea ni taa 50 tu ambazo haziko katika mtaa mmoja ambazo ni mbovu. Kwa hiyo, inawezekana barabara anayoisema inawezekana si barabara ambayo pengine inasimamiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS). Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama kuna changamoto ambayo mtaa mzima hauna taa nitaomba baada ya hapa tukutane naye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Ulyankulu tutakamilisha ujenzi na tutamwekea taa za barabarani 47 katika kituo chake hicho cha Ulyankulu, ahsante.
MHE. AMOUR KHAMIS MBAROUK: Mheshimiwa Spika,ahsante sana, na nimpongeze Waziri kwa niaba ya Serikali kwa majibu mazuri sana, ila nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, hizi kilometa 25172.42 zilizo bakia ambazo zimejengwa kwa changarawe zitajengwa lini kwa lami na zitatumia muda gani?

Swali la pili bajeti hii ya bilioni 1.8 ninavyoamini ni pamoja na kujenga michirizi au mifereji ya maji sasa kuna maeneo ambayo mifereji hii haijajengwa hata hapa Mjini Dodoma; je, ni lini mifereji hii itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo : -

Mheshimiwa Spika,kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, fedha inayokadiriwa kukamilisha mtandao wa barabara ambazo zinahudumiwa na TANROADS ni takribani tirioni 45; na bado barabara zingine zinaendelea kupandishwa daraja kuja, kwa hiyo zitaendelea kuongezeka.

Mheshimiwa Spika,na Serikali kusema ni lini tunaweza tukakamilisha ujenzi wa barabara zote kwa kiwango cha lami hii itaendelea kuwa ni kazi endelevu kadri fedha inavyopatikana. Kwa sababu, Mbunge atakubaliana nami kwamba bajeti tu ya nchi kwa mwaka ni zaidi ya tirioni 40 kwenda 41 kwa bajeti tunayoitekeleza sasa barabara hizi ni tirioni 45 kwa hiyo Serikali inajitahidi kujenga barabara kadri ya uwezo lakini hasa barabara zile za kipaumbele. Kwa hiyo kadri tutakavyoendelea tunahakikisha tutaendelea kupunguza idadi ya barabara za changarawe.

Mheshimiwa Spika,kuhusu swali lake la pili, ni kweli barabara zinajengwa lakini zingine hazina mitaro, lakini kipaumbele za kuweka mitaro hasa ni barabara ambazo ziko kwenye miji na maeneo ambayo wananchi wako wengi kwa ajili ya usalama. Na changamoto kubwa ambayo tunaipata kwenye uzibaji wa mitaro ni pale ambapo huduma za kijamii zinasababisha ile mitaro inaziba na basi maji hayo yanapanda kwenye barabara na kuharibu zile barabara.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, nini upi mpango wa Serikali katika ujenzi wa barabara ya Katoro – Kaseme – Magenge hadi Ushirombo?

Swali la pili; ni lini Serikali itapandisha kiwango cha barabara kutoka Geita – Buyagu – Kamena hadi Bukoli ili iweze kuhudumiwa na TANROADS ukizingatia kwamba maombi yake yamekwishafikishwa Wizarani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Katoro – Ushirombo imeshakamilishwa kufanyiwa usanifu, sehemu ya barabara hii pia tunao mradi wa RISE ambao kipande fulani kitatekelezwa kwenye mradi wa RISE ambao taratibu za manunuzi zinaendelea wakati Serikali inatafuta fedha kukamilisha barabara yote ya Katoro – Nyikonga hadi Ushirombo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili la barabara ya Geita – Nyankumbu – Kamena hadi Bukoli nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama imeshaletwa kwenye Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa ajili ya kupandishwa hadhi, Serikali itaangalia kama inakidhi vigezo ili barabara hii iweze kupandishwa hadhi na iweze kusimamiwa na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujua ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kuendeleza barabara ya Kiluvya – Kisarawe ikizingatiwa kuwa barabara hiyo inaiunganisha Wilaya ya Kisarawe na Makao Makuu ya Mkoa wa Pwani?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira tuone kwenye bajeti tunayotegemea kuileta mbele ya Bunge lako kama itakuwa na hiyo barabara. Nimhakikishie Mheshimiwa Serikali inatambua umuhimu mkubwa sana wa hiyo barabara kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa barabara hiyo inategemewa kiuchumi kutoa mazao sokoni, kupitisha watalii kwenda Mahale, na kwa kuwa mara nyingi Serikali imekuwa ikijibu upembuzi yakinifu, usanifu kwa muda mrefu, zaidi ya miaka mitano.

Je, Waziri anaweza akanihakikishia kabisa ni lini sasa barabara hiyo itaanza? (Makofi)

Swali langu la pili, kwa kuwa Kivuko cha Ilagala huanza kazi saa 12 na kuishia saa 12 na kinategemewa na Kata ya Sunuka, Sigunga, Helembe na Kalya, saa 12 mawasiliano yanakuwa yamekatika.

Je, kwa nini Serikali isiongeze muda kivuko kikafanya kazi mpaka Saa Sita usiku? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyoongea consultant kwa maana ya mhandishi mshauri yuko kazini kwa ajili ya kusanifu hilo Daraja la Malagarasi. Kwa hiyo tayari Serikali imeshaanza kufanya kazi, siyo tena hadithi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa ajili ya kuongeza masaa naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaangalia uwezekano wa kuongeza masaa kadri itakavyowezekana. Pia Serikali inaona suluhu ni kujenga daraja kwenye hicho kivuko na ndiyo kazi ambayo inafanyiwa usanifu ili badala ya kuwa na kivuko ambacho kinafanya kazi kwa masaa tujenge daraja la kudumu ambalo tutanfanya kazi muda wote.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri ni lini barabara ya Bujela – Masukulu hadi Matwebe itawekwa katika kiwango cha lami katika Wilaya ya Rungwe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira ya Serikali ni kujenga barabara zote za lami, tutashirikiana na wenzetu wa TARURA kuona kwamba hii barabara nayo inaingizwa kwenye usanifu na hatimaye iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri ni lini, kwa sababu kivuko hicho ambacho amekizungumza eneo hilo lina giza sana. Je, ni lini ataweka taa kwenye eneo hilo la kivuko?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge naomba nichukue wazo lako na tuangalie uwezekano wa kuweka taa kwenye hilo eneo la kivuko ambalo linaunganisha hizo pande mbili kwa ajili ya kusaidia kufanya kazi muda wa usiku.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Nangwa – Gisambala – Kondoa ikiwepo Daraja la Munguri kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja tuna mpango nayo kwa ajili ya kukamilisha na ku-review usanifu na baada ya hapo gharama zitajulikana ili tuweze kuipanga sasa kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mlowo – Utambalila mpaka Kamsamba kila kitu kiko tayari, nyaraka za tender, usanifu wa kina. Sasa nilitaka nijue, ni lini Serikali itapeleka barabara hii kwa Mheshimiwa Rais kuombewa kibali cha kujengwa kwa njia ya lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mlowo – Utambalila hadi Kamsamba ni barabara ambayo tayari Serikali imeshajenga Daraja la Mto Momba na kumekuwa na maelekezo ya viongozi mbalimbali wa Kitaifa akiwepo Waziri Mkuu, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaiweka kwenye mapendekezo kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa bajeti ambayo tunaiendea mbele.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana pamoja na majibu hayo mazuri ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa upembuzi yakinifu sasa umekamilika je, Serikali iko tayari sasa kutenga fedha kwenye bajeti hii tunayoijadili hivi sasa ya 2023/2024 kwa ajili ya kuanza rasmi ujenzi wa barabara hiyo ambayo inakwenda mpaka makao makuu ya halmashauri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili je, Serikali sasa iko tayari kufanya upembuzi yakinifu kwa kipande kinachounganisha barabara hii cha kutoka hapo Ilongero makao makuu ya halmashauri kupitia Ighanoda kwenda ngamu kilomita 27.1 ambayo inatuunganisha na Wilaya ya Hanang Mkoa wa Manyara? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwamba tumeshakamilisha usanifu wa hii barabara na sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha. Na nataka nisiji-commit hapa, kwamba kama bajeti tumeshatenga, lakini itategemea na upatikanaji wa fedha, kwa sababu baada ya kukamilisha usanifu kazi inayofata ni kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami; na ndiyo hiyo dhamira ya Serikali kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu barabara aliyoitaja ambayo inaanzia Ilongelo hadi Ngamo ni barabara fupi kama kilomita zisizozidi 27. Naomba nimuagize Meneja wa Mkoa afanye tathmini ya gharama kwa ajili ya kuanza kufanya usanifu kwa barabara hiyo, halafu aipeleke Makao Makuu kwa ajili ya kufikiria kuiweka kwenye mpango wa kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa hicho kipande cha barabara cha Ilongelo kwenda Ngamo, ahsante.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Kwanza napenda kuishukuru sana Serikali kwa ujenzi wa hii barabara kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Kwa kuwa Serikali imewekeza ujenzi wa bandari pale Karema, ujenzi ambao ni mkubwa sana: Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba barabara ya kutoka Kagwila kwenda Karema inafanyiwa ukarabati, kwani kwa sasa hivi imeharibika sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kumekuwa na matatizo watu wanapopisha ujenzi wa barabara, Serikali imekuwa na tabia ya kuchelewesha kuwalipa: Je, Serikali imejipanga vipi kuwalipa wananchi watakaopisha ujenzi wa barabara inayojengwa kwa kiwango cha lami toka Kagwila kwenda Karema?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nipokee shukurani kwa niaba ya Mheshimiwa Rais, kwa sababu shukurani hizo ni zake, ndiye anayetoa hizo fedha kujenga hiyo miundombinu. Kwa maswali yake mawili, nakubali kwamba barabara ya Kagwila kwenda Karema kilomita 112 inayoenda kwenye Bandari ya Karema ilikuwa na changamoto, lakini Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Mkoa kupitia Meneja, waliomba fedha za ziadam Shilingi milioni 500 tulishatoa, na wako wanakarabati maeneo yale ambayo yalikuwa hayawezi kupitika hasa maeneo ambayo wanalima mpunga karibu na barabara. Kwa hiyo, kwa sasa tunavyoongea, Mheshimiwa Mbunge barabara ile inapitika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu fidia, tayari tumeshakamilisha tathmini na wananchi wote ambao watalipwa kwa mujibu wa sheria zetu kwa barabara ya Kagwila hadi Karema, tayari wameshatambuliwa na tayari wameshajulishwa kila mtu atalipwa kiasi gani. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itawalipa wote watakaopisha barabara kwa mujibu wa sheria, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona. Barabara ya Nangulukulu - Liwale, inayopita katika majimbo ya Kilwa Kusini, Kilwa Kaskazini na Liwale, imeharibika vibaya kutokana na mvua za hivi karibuni. Nini maelekezo ya Wizara, kuelekeza TANROADS Mkoa wa Lindi kufanya marekebisho katika maeneo ya Nangulukulu - Migelegele – Mbate, Naiwanga – Njinjo – Miguluwe mpaka Kimambe?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kama tulivyosema huko nyuma na tulikwishatoa maelekezo na ninatoa sasa maelekezo mahususi kwa Meneja wa Mkoa wa Lindi, kuhakikisha kwamba anakwenda maeneo yote ya barabara ya Nangulukulu – Liwale kurekebisha maeneo yote ambayo hayapitiki kwa sasa na kama kutakauwa na changamoto ya kibajeti basi aweze kuwasiliana na TANROADS Makao Mkauu kwa msaada zaidi ili kuhakikisha kwamba anarejesha mawailiano.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Barabara ya Singida kupitia kwamtoro mpaka Kedashi - Tanga, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa nchi yetu na kwa sababu mlituambia tayari imekwishawekwa kwenye mpango wa kujengwa, na imetangazwa katika kilomita 2100. Ni lini sasa mkandarasi atakuja kwa ajili ya kuanza kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba barabara hiyo tuna mpango thabiti wa kuijenga kwa kiwango cha lami. Kama tulivyokuwa tunaelezea kwamba nitajengwa kwa mpango wa EPC+F na ninaomba Mheshimiwa Mbunge, avute subira ataisikia tutakapokuwa tunawasilisha bajeti yetu. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika,
ahsante sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni lini barabara ya Gairo hadi Milima ya Nongwe ambayo ni agizo la viongozi wa kitaifa, itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; barabara ya Ifakara – Mbingu – Chika – Mlimba ni mbovu sana; je, ni lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Gairo kwenda Nongwe ni barabara ya mkoa ambayo haijafanyiwa upembuzi yakinifu wala usanifu wa kina. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii TANROADS kupitia Mkoa wa Morogoro wameomba iwekwe kwenye upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa maana ya kufanya maandalizi ya kujenga kwa kiwango cha lami kwa mwaka huu wa fedha tunaouendea.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara aliyoitaja ya Ifakara - Mlimba - Kibena. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ya Awamu ya Sita tayari ilishatangaza barabara hii kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami, ambapo imegawanya katika lot mbili kuanzia Ifakara hadi Mbingu na Mbingu hadi Chita. Kwa hiyo, tayari iko kwenye hatua za manunuzi na tunategemea kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha barabara hii itakuwa pengine imeshaanza kujengwa, ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nashukuru sana Serikali kwa kuanza mchakato wa barabara hizi za kufungua Mkoa wa Morogoro. Sasa kipande cha Ifakara - Lupilo kimetangazwa.

Sasa swali langu la kwanza, je, ni lini kipande cha Lupilo – Mahenge – Liwale kitaanza ujenzi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kipande hiki cha Ifakara – Lupilo kitapita by pass ya Ifakara Mjini ambako wananchi wa Kata ya Mbasa na Katindiuka wamesubiri kwa muda mrefu sana, zaidi ya miaka minne kulipwa fidia na Serikali yao.

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hawa pamoja na hasara ya kusubiri zaidi ya miaka minne? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kipande cha Barabara ya Lupilo – Mahenge - Liwale kina sehemu mbili. Kwanza kuanzia Lupilo hadi Mahenge ni barabara kuu ambayo itakuwa ni sehemu ya ujenzi kwenye barabara hii kubwa ambayo nimeitaja kwa mpango wa EPC, lakini kuanzia Mahenge kwenda Ilonga hadi Liwale tumesema mwaka huu tumeingiza kwenye mpango wa kuanza kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu, maana hiyo barabara haipo lakini Serikali kwa sababu ya maombi ya muda mrefu kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Lindi tumeshaweka kwenye mpango wa kuanza kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu by pass ya Ifakara; hii by pass ya Ifakara ni sehemu ya huo mpango mkubwa na kitakachofanyika sasa ni pamoja na kuhuisha zile tathmini zilizofanyika kwa wananchi ambao wataathirika na mradi huu kwa ajili ya kuwalipa fidia. Kwa hiyo watakuwa ni sehemu ya huo mradi mkubwa ambao tunaenda kuutekeleza, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimshukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini swali la kwanza; ni lini upembuzi yakinifu na usanifu wa kina utafanyika kwenye daraja hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali ya Mozambique iko tayari kutoa ushirikiano wa ujenzi wa daraja hilo, ni lini mazungumzo haya yatakuwa yanaendelea kwa kina? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kutambua umuhimu wa barabara hii kwa upande wa Tanzania, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi upande wa Tanzania tuko tayari kuijenga hiyo barabara na katika mwaka huu wa fedha ambao tunakwenda kuleta bajeti, tumeweka fedha kwa ajili ya kuanza kufanya maandalizi ya kufanya usanifu na kufanya upembuzi na usanifu wa kina, lakini kama nilivyosema kazi hiyo itaanza tu pale ambapo tutakuwa tumekamilisha na wenzetu wa Msumbiji kwa sababu ni daraja la pamoja, ahsante. (Makofi)
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hiyo barabara ya Simbo – Kalya, hiyo barabara inaendelea mpaka Wilaya ya Tanganyika ambayo ni Kalya -Lugalaba, Bujombe yenye urefu wa kilometa 37 ambayo inaenda kwenye Wilaya ya Tanganyika katika Mkoa wa Katavi. Ni lini nayo itawekewa fedha kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha changarawe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika barabara hiyo hiyo, iko barabara ambayo ni ya Lukoma hadi Mwese, yenye urefu wa kilometa 47 ambayo nayo inakwenda nayo kwenye Mkoa wa Katavi. Naomba nijue, ni lini nayo itawekewa fedha kwa ajili ya ujenzi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambazo tunazihudumia sisi zinaishia Kalya, lakini ni kweli pia kwamba, kwa sababu tumeshawekeza eneo la Sibosye, tuna bandari yetu pale, kwa hiyo, tumefungua barabara mpaka Sibosye kwa ajili ya kuhakikisha kwamba hiyo bandari inafanya kazi, na tutaendelea kwa barabara ambayo inaenda Katavi. Pia kwa upande wa Kigoma tumeshaifungua mpaka mpakani mwa Katavi, na wenzetu wa Katavi pia wameshaanza kutenga fedha kuifungua ili hizo barabara ziweze kuunganishwa ambapo itatumika pia kama barabara ya ulinzi kwa mikoa hiyo miwili ya Katavi na Mkoa wa Kigoma, ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kipande cha barabara ya lami kutoka Mbulu Garbabi, kazi ya Mkandarasi imesimama kwa miezi minne; je, ni lini mkandarasi yule ataanza kazi ile rasmi ili barabara hiyo iweze kutekelezwa kwa wakati na kwa mujibu wa mkataba?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara anayoisema hii, ni kweli kulikuwa kuna changamoto ya mvua na pia mkandarasi alikuwa hajalipwa fedha zake alizokuwa anadai. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunavyoongea sasa hivi mkandarasi ameshaanza kazi ya Mbulu kwenda Garbabi na tunategemea muda wowote kuanzia sasa tutasaini mkataba wa Labay kwenda Haydom, ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Tunaishukuru sana Serikali kupitia Wizara ya Ujenzi kwa kusukuma sana ujenzi wa barabara ya Sanzate – Nata; je, ni lini kipande cha Nata mpaka Mugumu ujenzi wake utaanza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Nata kwenda Mugumu ni barabara ambayo tutakuwa tunakamilisha barabara ya makutano Nata hadi Mugumu. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti ambayo tunaiendea, tumeipanga ili iweze kukamilika na hivyo kukamilisha mzunguko wa Nata – Mugumu; Mugumu hadi Tarinya kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Mlowo – Utambalila mpaka Kamsamba, nyaraka za tenda, usanifu wa kina, kila kitu kipo tayari, na ipo ndani ya mpango wa bajeti: Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili ujenzi wa kiwango wa cha lami uanze kwenye hiyo barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwenisongole, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Mlowo - Utambalila hadi Kamsamba, barabara ambayo Mheshimiwa Mbunge amekuwa anaiulizia mara kwa mara, tumemhakikishia kwamba hiyo barabara ambayo inaunga Mkoa wa Songwe na Rukwa, tumeiweka kwenye mapendekezo, na tuliagizwa pia na viongozi kwamba barabara hiyo sasa tuanze kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tusubiri bajeti kama itapitishwa, barabara hiyo tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Majibu aliyoyatoa yako sahihi na kama yatatekelezeka, Meatu tutafaidika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mpango huu wa kujenga madaraja haya kwa kupitia barabara hiyo ya lami itakuwa ni mwezi Oktoba: Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kujenga madaraja haya kwa muda mfupi, Lyusa pamoja na Chobe ili wananchi wa Meatu waendelee kutumia ile barabara kwa mwaka mzima? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Minza yote kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, haya madaraja ni madaraja aina ya drift, na katika mpango ambao tutaujenga sasa kwa mpango mkubwa wa EPC+F, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, tunategemea mradi huu usainiwe kabla ya mwisho wa mwezi Juni. Kwa hiyo, tumejumuisha hayo madaraja, yatajengwa wakati huo mradi mkubwa unatekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri haya ya Serikali. Lakini naomba nikupongeze wewe mwenyewe kwa jitihada hizi na sasa kweli maendeleo ya Mbeya na Mbeya imetulia. Swali langu la kwanza je, ni lini sasa wananchi waliyopisha hii barabara wataanza kulipwa fidia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Kuna barabara ya kiungo muhimu cha Mkoa wa Songwe pamoja na nchi jirani ya Malawi. Barabara ya Mbalizi – Shigamba ni lini Barabara ya Mbalizi – Shigamba itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kwamba barabara hii itaanza kujengwa kwa EPC+F ili kupunguza msongamano katika Jiji la Mbeya. Hii inaenda sambamba na ujenzi wa barabara ya njia nne kilomita 29 Uyole hadi Ifisi ambayo tayari Mkandarasi yuko site. Sasa kuhusu fidia ni kwamba fidia itaanza kulipwa mara tutakapokuwa tumehakiki wale wananchi wote ambao walishaainishwa kwamba watalipwa kwa mpango wa sasa kwamba kabla atujaanza kujenga hiyo barabara tutahakikisha kwamba fidia inalipwa kwenye barabara hiyo ambayo wananchi watapisha ujenzi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala lake la pili Barabara ya Mbalizi – Shigamba ambayo inakwenda mpaka Itumba – Isongole mpakani na Malawi. Nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba sasa hivi tunakamilisha na anafahamu Mheshimiwa Mbunge tunakamilisha kufanya usanifu wa kina na tunategemea mwaka huu tutakamilisha na baada ya hapo sasa utaratibu ni kuijenga barabara hiyo yote kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa ahsante, zabuni ya ujenzi wa kilometa nane za awali kwa Barabara ya Dareda – Dongobesh imetangazwa zaidi ya mara mbili. Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo itaanza kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kweli tulishatangaza lakini tumeitangaza tena nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba barabara hii kilomita zote zilizotangazwa kilomita 8 tutaijenga katika kipindi hiki shida ilikuwa tu baada ya kutangaza hatukumpata mkandarasi sahihi. Kwa hiyo, mpango upo na tayari tumeishaitangaza upya na tuko kwenye mazungumzo na mkandarasi ambaye ataijenga. Kwa hiyo, tutakapokuwa tumeikamilisha hayo mazungumzo barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, Serikali inaniletea majibu siyo sahihi. Barabara niliyouliza mimi ni ya kutoka Mangaka – Nachingwea – Liwale hadi Mahenge, iko ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu. Napatiwa majibu ya Wilaya nyingine ambayo mimi sijauliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali iko tayari kurudi ikajipange upya iniletee majibu sahihi ya swali langu? Hilo la kwanza.

Swali la pili, barabara ninayoiuliza mimi ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, alipokuja ndani ya Jimbo langu mwezi Oktoba, 2020. Je, Serikali inatuambia nini juu ya ahadi hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara aliyoisema ya kutoka Mangaka – Kilimarondo ambayo inaunganisha na Mkoa wa Morogoro, sehemu ndogo inahudumiwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, lakini sehemu kubwa inahudumiwa na wenzetu wa barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana naye kwamba pia yalikuwa ni maelekezo ya viongozi wa Kitaifa kwamba barabara hiyo ijengwe. Kitu cha kwanza ambacho tutaifanya ni kuipandisha hadhi ile barabara – Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami, kuipandisha hadhi ije TANROADS tufanye upembuzi yakinifu na usanifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichosema kuhusu barabara niliyoitaja, ni barabara ambazo zinakwenda sambamba, ukitoka Masasi – Nachingwea kwenda Liwale hii barabara inakwenda sambamba na barabara ya kutoka Mangaka – Kilimarondo kwenda Liwale. Sasa hiyo kwa kuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba itapandishwa hadhi halafu itakuja TANROADS tutafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili kuijenga hiyo barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Sumbawanga – Mpanda imetengenezwa kimebakia kipande kidogo cha kutoka Chala – Mpalamawe.

Je, ni lini hiki kipande kitajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kipande hiki alichokisema cha Chala – Mpalamawe, kimsingi ndiyo barabara kuu, lakini kwa sababu Makao Makuu ya Wilaya ya Nkasi yako nje ya barabara kuu, Serikali iliona ni busara barabara ya lami badala ya kujengwa huko porini ipite Makao Makuu ya Wilaya ambayo ndiyo inaunganisha pale Mpalamawe kwenda Mpanda. Mpango ni kuja kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami ili kukamilisha hiyo barabara kuu pia, ahsante. (Makofi)
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza ninaishukuru Serikali kwa majibu mazuri sana, kwamba tayari kandarasi imeshatangazwa, pamoja na majibu hayo nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, tangu 2019 daraja lilipokatika walitengeneza diversion ambayo magari yote yalikuwa yanapita pale lakini kwa bahati mbaya sasa ile diversion imeharibika kabisa.

Nini mkakati wa Serikali wa kuimarisha hiyo barabara ya mchepuo?

Swali la pili, katika barabara hiyo kutoka Kijiji cha Kalema Maziwani mpaka Mondo, mkandarasi aliyepewa kazi ya kuweka mifereji aliweka chini ya kiwango na hivyo kipindi cha masika maji yale yanaharibu kabisa barabara. Nini kauli ya Serikali juu ya mkandarasi huyu? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu diversion naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa tayari tumeshatangaza tenda na Mkandarasi atakwenda site ni wazi pia kwamba wakati anajenga lazima hiyo diversion aiimarishe. Kwa hiyo, pia nitoe maagizo na maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dodoma kuhakikisha kwamba anakwenda kuimarisha hiyo diversion ili wananchi na wasafiri wanaopita pale waweze kupita sehemu salama ambapo sasa ni kiangazi, naamini ataitengeneza hiyo diversion.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mifereji. Ni kweli barabara hii tunatengeneza mifereji kwa awamu, tumeendelea kutenga bajeti na hata mwaka huu wa fedha tunakokwenda mifereji itaendelea kutengenezwa. Kwa hiyo, pia nimuagize Meneja wa Mkoa wa Dodoma, kwamba kipindi hiki cha kiangazi ndicho kipindi sahihi cha kutengeneza mifereji, pia niwaombe wananchi wa Chemba kutokufanya shughuli za kijamii karibu na barabara na kuweza kusababisha baadhi ya mifereji kuziba na kuleta changamoto kwenye miundombinu ya barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa hii nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Manyoni Mashariki kuna Daraja la Sanza ambalo upembuzi yakinifu, usanifu wa kina na ulipaji wa fidia wananchi ulishakamilika. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Sanza? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli daraja la Sanza ni kati ya madaraja makubwa ambayo yanaunganisha Mkoa wa Singida na Mkoa wa Dodoma na Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba tulitangaza tenda lakini bahati mbaya sana, Mkandarasi aliyepata hiyo tenda alijitoa na sasa tunaendelea na negotiations na Mkandarasi wa pili kwa maana ya kulijenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo daraja lilikuwa limepangwa actually liwe limeanza kujengwa katika mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira hiyo ipo, tunaendelea na negotiations na yule mshindi wa pili ili aweze kuanza kulijenga hilo daraja. Ahsante.
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Naibu Waziri, ninaomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, ninataka nijue barabara hizo unganishi ambazo zimejengwa kwa kiwango cha lami ni zipi.

Swali langu la pili, barabara hii ya Mlowo – Kamsamba imekuwa na changamoto kubwa sana kwa wananchi wetu, lakini changamoto hizi zinatukosesha fursa muhimu za kiuchumi. Nataka kujua Serikali ina mkakati gani wa maksudi kuhakikisha inajenga barabara hizi kwa wakati na muda muafaka ili kuondoa changamoto ambazo wanakutana nazo wananchi wa Mkoa wa Songwe, Momba na maeneo mengine kwa ujumla. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nimemuelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichokuwa nasema tumeanza kuijenga, tuna Daraja la Mto Momba ambalo liko katika hiyo barabara, katika hilo daraja tumejenga approach roads ambazo zinaunganisha lile daraja ukitokea Mkoa wa Songwe na Mkoa wa Rukwa. Kwa hiyo, kwa pande zile mbili tayari kuna lami upande huu na huu, zile ndiyo barabara unganishi na lile daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la maksudi, kwamba je, tuna mkakati gani kuhakikisha kwamba tunajenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Bajeti inaendelea, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imetenga fedha, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, kwamba tutaanza kuijenga hiyo barabara ili kukuza uchumi pia kurahisisha usafiri kwa wananchi wa Mkoa wa Songwe wa Mlowo, Igamba, Utambalila, Kamsamba lakini pia Utambalila kwenda Makao Makuu ya Mji wa Momba ambayo ni Makao Makuu ya Wilaya. Ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi. Hii barabara ya Kibena – Lupembe – Madeke mpaka Morogoro ni barabara ya Kimkoa na ni kero ya muda mrefu ya wananchi wangu. Tarehe 19 Bungeni hapa Serikali iliahidi kuanza ujenzi wa kilometa 25 na sasa tuko kwenye bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Naomba kauli ya Serikali barabara hii inaanza ujenzi lini? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge ni kweli ni barabara inayounganisha Mkoa wa Njombe na Mkoa wa Morogoro, pia yalitolewa maelekezo maalum na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwamba barabara hiyo ni lazima ianze kujengwa. Nami nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Jimbo la Lupembe kwamba katika bajeti hii tayari tumeshaanza taratibu za kuanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, na tutaanza na kilometa 25 kwa kuanzia upande wa Mkoa wa Njombe, upande wa Morogoro tayari tuna kilometa 100 ambazo zinaendelea kujengwa na ziko kwenye taratibu za manunuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipande kilichobaki African Development Bank watakifanyia usanifu ili barabara yote iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimwia Mwenyekiti, Great Nyerere Road ni barabara muhimu sana kwa utalii wa Selous. Nimeona kwenye mapendekezo ya bajeti zimetengwa shilingi bilioni mbili ambayo ni sawa na kilometa mbili. Ni lini sasa Serikali itaanza kutenga fedha za kutosha ili tupate kilometa za kutosha kwa kuzingatia umuhimu wa barabara hii? ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa mpango wa bajeti kiasi tulichotenga aangalie kilometa ambazo tuna mpango wa kuzijenga. Ni azma ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii ya Kisarawe – Maneromango kwenda Hifadhi ya Taifa ya Nyerere yote inakamilika kwa kiwango cha lami. Ndiyo maana katika bajeti hii tumeshaweka fedha kuendelea na ujenzi wa hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hii ni mara ya tatu kama siyo ya nne tunauliza swali hili tunaambiwa kwamba Serikali itatafuta fedha. Tunaomba kauli ya Serikali, ni lini fedha itapatikana? Hii ni ahadi ya Rais toka mwaka 2005 mpaka leo fedha za upembuzi yakinifu na usanifu wa kina hazijapatikana? Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Kata ya Mhezi, Mshewa na Msindo, barabara hii inaponyesha mvua kidogo inaharibika sana kiasi ambacho magari hayapiti kabisa. Kwa hiyo, mawasiliano yanafungwa kati ya Kata hizo na Same: Je, ni lini Serikali itaweka zege katika barabara hiyo kwa maeneo hayo niliyoyataja kabla ya upembuzi yakinifu na upembuzi wa kina kukamilika ili barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, tunatambua umuhimu wa barabara hii na ndiyo maana katika jibu la msingi nimesema tunaendela kutafuta fedha kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri barabara hii mimi nimetembelea yote na tulishatoa maagizo na tayari tumeshaainisha maeneo yote korofi likiwemo eneo hilo la Msindo, Mshewa na Mhenzi. Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro ameshatengeneza bajeti na hivi ninavyoongea amesha-submit kwa Mtendaji Mkuu wa TANRIOAD ili aweze kutoa fedha kujenga hayo maeneo korofi ama kwa lami nyepesi ama kwa zege ili barabara hii iweze kupitika yote kwa mwaka mzima, ahsante.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya Msongola – Mbande nilipewa ahadi kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 itakamilishwa yote kilometa 4.95 kwa kiwango cha lami. Naomba commitment ya Serikali kutimiza ahadi hii iliyotolewa mwaka 2022 hapa Bungeni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara aliyoitaja ambayo inaanzia Pugu – Mvuti – Msongola – Mbande inaunganisha majimbo mawili; Jimbo la Mheshimiwa Silaa na Jimbo la Mbagala la Mheshimiwa Chaurembo. Tuna kilometa nne point ambazo bado hazijakamilika. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti tunayokwenda kuitekeleza tutakamilisha kwa lami kipande kilichobaki, ahsante. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kiwango cha lami barabara inayotoka Kahama – Busangi – Chela – Nyang’wale mpaka Busisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja tunakamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa maana ya kutoka Kahama kwenda Busisi. Pia, baada ya hapo ndiyo tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Galapo, Orkasmet hadi Kibaya Kiteto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, tunapoongea sasa hivi, barabara aliyoitaja ndiyo tunakamilisha usanifu wa kina na baada ya hapo tutatafuta fedha kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mwili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Je, ni lini ujenzi huo wa mita 500 utaanza?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Barabara hii ya lami inapita katikati ya Mji na ndiyo kwenye sura ya Wilaya ya Tunduru: Je, ni lini Serikali itatufungia taa za barabara ili kusaidia ulinzi na usalama nyakati za usiku? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mita 500, tunavyoongea mkandarasi ameshapatikana na sasa hivi anajiandaa, yuko kwenye mobilization kuanza kujenga hizo mita 500 kwa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, habari njema kwamba mwaka ujao katika huo mji ambao taasisi zote zinapita katika barabara ya TANROADS, tutajenga kilometa 2.1 na kuweka taa eneo lote katika mji huo wa Tunduru, ahsante. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika barabara ya Tunduru – Nalasi, kipande cha kutoka Chiwana mpaka Mbesa kina matatizo ya kupitika wakati wa mvua: Je, ni lini Serikali itaweka lami nyepesi kwenye kipande hicho wakati wanasubiri fedha za kujenga kipande hicho?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu langu la msingi na barabara hii niliitembelea, Waziri alishaahidi na mimi nilipita. Maeneo yote korofi tumeyaainisha na tumetoa maelekezo kwa Meneja wa Mkoa wa Ruvuma kwamba barabara hii yenye urefu wa kilometa 300 maeneo yote ayafanyie kazi kwa maana ya kuainisha maeneo korofi na pia kujenga kwa kiwango cha zege ama lami maeneo yote korofi ili barabara hii iweze kupitika kwa mwaka mzima, ikiwa ni pamoja na eneo alilolitaja Mheshimiwa Mbunge, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, barabara ya njia nane kilometa 19.2 kutoka Kimara hadi Kibaha, imekosa kabisa vituo vya dala dala kwa abiria kupumzika; kwa hiyo, wanaumia na jua na mvua: Je, ni lini Serikali itatengeneza hivi vituo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Japo suala hili Mheshimiwa Mbunge amekuwa akilileta mara kwa mara, lakini nimhakikishie kwamba pia Kamati ya Miundombinu imeshatoa maelekezo kwa Wizara kuhakikisha kwamba suala hili inalifanyiwa kazi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tumeshaliona na tayari Wizara imeshalipokea kwa ajili ya kutengeneza hivyo vituo kama alivyovitaja Mheshimiwa Mbunge, ahsante sana.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. lakini barabara inayofanana na Gairo kwenda Nongwe ni barabara ambayo inaanzia Ruaha Mbuyuni – Malolo – Mlunga – Reli Ng’ombe mpaka Kibakwe – Mpwapwa. Barabara hii imeshapitishwa na RCC kwa miaka miwili sasa; Je, nini kauli ya Serikali?

Mheshimiwa Spika, kutokupitisha barabara hii kwa kadiri ya maombi ya RCC mkoa wa Morogoro; Je, Serikali haioni kwamba inawapotezea haki wananchi hawa ambao wanasafiri mwendo zaidi ya kilomita 400 kufika Mpwapwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Londo Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii inaunganisha mikoa ya Morogoro, Iringa na Dodoma na Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba kwa sasa barabara hii inahudumiwa na wenzetu wa Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini, na atakuwa pia anaelewa kwamba baada ya kupokea maombi kuipandisha barabara hii ili ihudumiwe na TANROADS, wataalamu wameshaitembelea ili kufanyia tathmini na kuona kama inakidhi vigezo vya kuhamishiwa TANROADS. Kwa hiyo tayari maombi yameshafika Wizarani kwa ajili ya kufanyiwa tathmini na maamuzi, na baada ya hapo tutawajulisha kama imekidhi vigezo ili iweze kupanda hadhi, ahsante. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya kwenda Ruaha

kutoka Iringa Mjini iliahidiwa kwamba tutatangaza mwezi wa sita, mpaka sasa haijatangazwa; je, tutatangaza lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kulikuwa na taratibu zilikuwa bado hazijakamilika lakini zinakamilika, na baada ya hapo hiyo barabara itatangazwa ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, tarehe 5, mwezi wa Nane Wizara ilisaini barabara ya kutoka Ifakara kwenda Mbingu na baadaye Mlimba. Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hiyo itaanza kujengwa mara tu tutakapokuwa tumekamilisha taratibu zote ikiwa ni pamoja na mkandarasi kuanza kufanya mobilization, yaani kuandaa vifaa kwa ajili ya kuanza kuijenga hiyo barabara. (Makofi)
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika; je, Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga Barabara ya Hydom – Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara hiyo ilishafanyiwa usanifu na Serikali inatafuta fedha kuijenga hiyo Barabara ya Hydom Mogitu kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, Barabara ya Msongola – Mbande kilometa 4.95, ujenzi wa kilometa 1.5 una suasua. Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha ujenzi huo pamoja na kilometa 3.45 za kumalizia kwa lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba tu nichukue nafasi hii kumuelekeza Meneja wa TANROADS wa Mkoa wa Dar es Salaam kumsisitiza mkandarasi kwa sababu yuko site ili barabara hiyo iweze kukamilika ili tuondokane na hiyo vumbi ambayo ina kilomita kama 3.2. Hivyo tutakuwa tumeunganisha barabara yote kwa kiwango cha lami. Ni kumsisitiza tu meneja amsimamie mkandarasi kwa ukaribu. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa upembuzi yakinifu nimekuwa nikijibiwa kila mara kwamba utakamilika. Upembuzi huu ni kwaajili ya barabara kutoka Kahama – Nyangh’wale – Busisi. Je, ni lini upembuzi huo utakamilika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, barabara hii ni ndefu na upembuzi unaendelea kadiri muda unavyokwenda, ni kwamba tu hatuwezi tukaruka hatua. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakamilisha upembuzi na baada ya hapo hatua zitakazofuata itakuwa ni kutafuta fedha kujenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, Barabara ya Bugene, Nkwenda mpaka Isingiro inasababisha ajali kwa sababu ya vumbi kubwa; Je, ni lini ujenzi wake utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante; labda tu cha kwanza ni kuhakikisha kwamba kama kuna vumbi ndiyo barabara zilivyo za vumbi, lakini Serikali imeendelea kutafuta fedha kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Pakiwa ni barabara ya vumbi haiepukiki, lakini Serikali inaendelea kutafuta fedha kuzijenga hizo barabara kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kupunguza ajali kwenye maeneo husika. Ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tukuyu Mjini kuna barabara ya lami inayojengwa kule njia ya kwenda Masoko, tunashukuru. Barabara ile mkandarasi ameweka kifusi kikubwa maeneo ya Ranbos kuelekea Mpindo; sasa, je, ni lini mkandarasi yule atasawazisha kifusi hicho ili wananchi wa Mpindo wapite vizuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, haya ni maelekezo tu kumuelekeza; namuelekeza Meneja wa Mkoa wa Mbeya wa TANROADS kuhakikisha kwamba anamsimamia mkandarasi huyo kuondoa kifusi na kukisawazisha haraka inavyowezekana. Ahsante.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, barabara ya Kamanga – Sengerema imetangazwa kwa ajili ya ujenzi wa lami;

Je, ni lini mkandarasi atakuwa site kwa ajili ya kuanza kazi ya ujenzi wa Barabara ya Kamanga – Sengerema?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa barabara hiyo ni kwa mwaka huu kwa hiyo taratibu zinaendelea, zikishakamilika barabara hiyo itatangazwa kuanza kujengwa, ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ni miezi mitatu sasa Barabara ya Masasi – Nachingwea mkataba ulisainiwa;

Je, ni lini ujenzi wake utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara kama nimemsikia Masasi – Nachingwea – Liwale ni barabara ambazo ziko kwenye EPC+F na taratibu za kuzijenga hizi barabara zote zinaendelea, ikiwa ni pamoja na kuangalia maeneo ya kujenga makambi, kuvigawa vipande ambavyo vitatumika kujenga hizo barabara lakini pia mkandarasi kupitia upya usanifu na kuangalia fidia ambazo zitalipwa kwa wananchi ambao wataathirika na ujenzi. Kwa hiyo taratibu zimeshaanza na zinaendelea. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante; Barabara ya Mugakorongo – Kigalama mpaka Mrongo mkandarasi alishapatikana; ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara ambazo zilitangazwa kwamba zitakuwa zimesainiwa, barabara anayoisema tayari mkandarasi alishapatikana na taratibu zinafanyika kwa ajili ya barabara hiyo, kuanzia upande wa Mrongo. Tunachosubiri sasa hivi ni kufanya signing na kumkabidhi mkandarasi site ili aanze kijenga. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; Barabara ya kutoka Namtumbo – Mtonya – Mgombasi kuna daraja linalohatarisha usalama wa watu na mali zao;

Je, ni lini daraja hilo sasa litakarabatiwa katika Mto Luwegu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, nimuagize Meneja wa Mkoa wa Ruvuma kwenda kulitembelea hilo daraja; na kama daraja hilo halijatengewa fedha za matengenezo aweze kuleta tathmini ili tuondokane ama tusije tukapata ajali. Atuletee Wizarani gharama na tuweze kulikarabati daraja hilo. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, katika maswali ya kuangalia sana ni hili swali. Tumeona Serikali ikiwa ikivamia wananchi kwenye maeneo yaliyovamiwa na Serikali wanabomolewa nyumba zao. Miaka 14 sasa wananchi takriban nchi nzima maeneo yale ambayo ni maeneo nyeti ya barabarani yamekaliwa na Serikali bila fidia, bila kwenda kuyapima. Sasa swali langu lilikuwa linahusu;

Je, ni lini Serikali itatoa tamko la wananchi kung’oa vila vigingi na kuingia kufanya maeneo hayo kwa shughuli za maendeleo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imesema kwamba maeneo ambayo yamechukuliwa toka 2009 mpaka leo, kuna mengine yatafidiwa kuna mengine kuna hayatafidiwa;

Je, wale ambao hawatafidiwa wako tayari kupewa hela ya usumbufu, kwa maana ya fidia ya usumbufu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya kuliona hili tatizo katika bajeti ambayo tumepitishiwa ya mwaka huu wa 2023/2024 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kufanya tathmini, na hili linapatikana kwenye ukurasa wa 194 wa kitabu chetu. Tumeeleza hili suala na changamoto yake ambayo ipo. Na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba wale ambao wako ndani ya mita 7.5 nyumba zao hazijabomolewa; ila ziliwekwa alama ya X ya kijani ikionyesha kwamba barabara imewafuata na wanastahili fidia. Kwa hiyo kwa sababu ya nchi nzima ndiyo maana Serikali imekuja kufanya tathmini ione ni maeneo yapi ambayo kweli sasa tutayahitaji na yatafidiwa, na yale ambayo hatutahitaji kwa sasa wananchi wataruhusiwa waendelee kuyatumia baada ya kufanya hiyo tathmini.

Mheshimiwa Spika, hao wa usumbufu nadhani sheria zetu na kanuni zetu za namna ya fidia inavyofanyika zitatumika ili kuona namna ya kuwafidia wale ambao watakuwa wamepata huo usumbufu, ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Mkoa wetu wa Lindi barabara zetu kuu na barabara za mikoa zina changamoto hii kubwa ya kuwepo kwa vigingi katikati ya makazi ya wananchi;

Je, ni lini Serikali italipa fidia ili wananchi waendelee na shughuli zao kama kawaida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, suala hili linafanana sana na suala la msingi na jibu langu litaendelea kubaki kwamba; ndiyo maana katika bajeti hii tumetenga fedha kwa ajili ya kufanya tathmini, na kama ni maeneo ambayo tunayahitaji kwa sasa tutakuja tuwafidie halafu tuweze kujenga hizo barabara ama kuacha hiyo corridor ikiwa wazi baada ya kuwaondoa wananchi kwa kuwafidia likiwa ni pamoja na hilo la eneo la Mheshimiwa Mbunge ambalo amelisema. Ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuna baadhi ya maeneo unakuta kwamba jiwe la TANROADS limewekwa zaidi ya mita 30 kama ambavyo umetuhabarisha hapo;

Je, katika mazingira hayo TANROADS watakuwa tayari kuondoa mawe hayo kwa gharama zao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama ni barabara ambayo imesanifiwa maana yake ni kwamba pale ilipo ndipo zinapoishia mita 30, na maana yake ni kwamba pale ilipo barabara ambayo ipo itasogea upande huo ili kufikisha mita 30. Hao watakuwa watafidiwa pia kwa sababu barabara itakuwa imehama kutoka ilipokuwa na kusogea upande huo wa kwenye kigingi, ahsante.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza sikubaliani na majibu yaliyotolewa na Serikali na swali hili limerudi kwa mara ya pili baada ya maelekezo ya Mheshimiwa Spika wakati fulani hapo nyuma kwa sababu zifuatazo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili tunalolizungumzia barabara ilihama kwenye original plan na barabara hii imewafuata wananchi. Kwa sababu hiyo haina qualification ya mita 22 wala mita hizo zinazotajwa 22.5 wala nyongeza ya mita 7.5. Mheshimiwa Waziri Mbarawa alifika kwenye hiki kijiji tarehe 22 mwezi wa kwanza, mwaka 2022 eneo ambalo Misikiti, Kanisa pamoja na Nyumba za Serikali zilivunjwa. Swali langu la msingi ni lini Serikali itakwenda kulipa fidia kwa sababu wenyewe walifuatwa na barabara na si wao waliifuata barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi; kwamba kama barabara imemfuata mwananchi ama imehama na kwenda sehemu ambayo haikuwepo maana yake hawa watu wanastahili fidia; na kama suala alilolielezea Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara imehama kabisa. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wananchi hawa watakuwa wanastahili fidia. Kwa hiyo, kwa sababu swali lake ni specific na eneo linalohusika, naomba baada ya hapa tuweze kukutana naye ili tuweze kuangalia. Kama barabara iliwafuata hawa wananchi kama alivyosema basi wananchi hao wana haki ya kulipwa fidia. Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza;

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi waliopisha Barabara ya Mianzini – Sambasha - Kimyaki hadi Ngaramtoni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii ni mpya na imefunguliwa. Tayari tulishandaa taratibu za kuwalipa wananchi ambao tumeifungua ile barabara, na barabara iliyoanza ni mpya wananchi hao watalipwa mara baada ya kukamilisha taratibu zote za fidia, ahsante. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa tangu tathmini ya malipo ya fidia kwa wananchi wa Nanganga yamefanyika muda mrefu umepita.

Je, Serikali iko tayari kuongeza kiwango cha fidia kwa wananchi wale kwa sababu walisimama kabisa katika maendeleo yao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni utaratibu wa Serikali kwamba kama fidia imefanyiwa tathmini ikapita miezi sita ni lazima turudi kuhuisha tena ile tathmini ili kupata thamani ya wakati huo. Kwa hiyo itafanyiwa tathmini mpya kama imepita miezi sita na watalipwa sasa fidia ya wakati huu, ahsante. (Makofi)

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Napenda kuuliza barabara ya Bypass ya Uyole – Songwe, ni lini wananchi watalipwa fidia waliopisha hiyo barabara ya bypass?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE.ENG GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara inayotajwa ndiyo kwanza wakandarasi wameshakabidhiwa, na ipo kwenye huu mpamgo wa EPC+F. Jana nilijibu kwamba moja ya vitu ambavyo sasa hivi vinafanyika ni kupitia upya na kufanya tathmini ya malipo yatakayofanyika kwa ajili ya wale wananchi ambao watapisha, ikiwa ni pamoja na wananchi wa hiyo Barabara ya Uyole – Songwe Bypass. Ahsante.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Barabara ya Makofia- Mlandizi – Mzenga mpaka Vikumbulu miaka mitatu iliyopita walifanyiwa tathmini ya kilomita 30 na miezi miwili iliyopita wamerudi kubadilisha kurudi kwenye mita 22.5;

Je, ni lini wananchi wale watalipwa fidia pamoja na mabadilko hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, tayari tumekwenda kwa ajili ya kufanya tathmini kwa watu ambao wapo ndani ya mita 22.5. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba maandalizi yanafanyika ndiyo maana tumekwenda sasa hivi ili waweze kulipwa fidia. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika pamoja na majibu mazuri ya Waziri barabara hii ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya 2020/2025 na huenda pia kwenye Bajeti iliyopita Waziri aliliahidi Bunge hili kuwa atatenga fedha kwenda kuanza usanifu katika barabara hii;

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha ili wananchi hao waanze kufanyiwa usanifu ili barabara yao ijengwe?

Mheshimwa Naibu Spika, swali langu la pili, barabara ya Chaya – Nyaua, Chanya – Manyoni – Tabora yenye kilomita zaidi ya 200, sasa kumekuwa na msongamano wa magari mengi. Tuliomba pendekezo la kuiweka bypass ya Kigwa – Magili;

Je, ni lini Serikali itaanza usanifu wa kuiweka barabara ya Kigwa- Magili ili iweze kupata kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika kama nilivyosema, barabara hii ya Chimo – Simbo hadi Puge ilikuwa haijafanyiwa usanifu; na tayari tumeshaanza kufanya usanifu. Wakati wa Bajeti ni kweli Waziri aliahidi kwamba tutaanza kujenga kilomita 10 kwa kiwango cha lami, lakini kilomita hizi zitaanza kujengwa pale tu ambapo usanifu utakuwa umekamilika, hizo kilomita za awali kilomita 10. Barabara ya pili Serikali inaendelea kutafuta fedha ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami kama alivyoomba Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumuuliza swali Mheshimiwa Naibu Waziri. Barabara ya Kenyatta itokayo Mwanza Mjini kwenda Shinyanga ambayo tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na umeshakamilika, pia usanifu umekamilika. Barabara imezidi kuwa na msongamano mkubwa;

Je, ni lini sasa Serikali itahakikisha barabara hii inapanuliwa kwa njia nne? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE), Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli moja ya barabara katika majiji ambayo sasa hivi ina magari mengi ni hiyo Barabara ya Kenyatta kwenda Usagara kuelekea Shinyanga. Serikali imeshafanya usanifu na sasa hivi inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga barabara hiyo kwa njia nne ili kupunguza changamoto kubwa ya foleni katika Jiji la Mwanza, ahsante. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Kaoze- Chombe kwenda Igonda iliyopo Sumbawanga Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE.ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii bado hatujaiingiza kwenye mpango wa kuijenga kwa mwaka huu. Lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla ya kuanza kuijenga tutatafuta fedha kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina katika bajeti inayokuja, siyo kwa bajeti hii; kwamba hatukuipangia fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Ni lini mkandarasi wa kujenga Barabara ya kutoka Iringa Mjini kwenda Kilolo ataweka saini mkataba na kuanza ujenzi? Kwa sababu limekuwa ni jambo la muda mrefu na wananchi wanasubiri kwa hamu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii kwanza inafadhiliwa na World Bank, na fedha zipo. Kinachoendelea sasa hivi ni kukamilisha tu taratibu kati ya Serikali na mkandarasi ambaye tayari alishapatikana ili aweze kukabidhiwa hiyo site kujenga hizo kilomita 33 za Iringa kwenda Kilolo.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara ya Mafinga - Kihansi inaungana na barabara ya Ifakara – Mlimba - Madeke mpaka Njombe Kibena junction, ninaishukuru Serikali kwa kuwa mwaka huu wa fedha bajeti ilitengwa ujenzi wa kiliometa 100 ianze kujengwa barabara hii ya Ifakara – Mlimba – Njombe, mpaka sasa taarifa nilizonazo mkataba umeshasainiwa ujenzi wa kilometa 62.5 uanze kujengwa. Swali langu dogo hapo ni kwamba; je, ni lini sasa mandarasi atakabidhiwa site na ujenzi uanze mara moja? (Makofi)

Kwa kuwa, barabara hii kwa mujibu wa bajeti ilitengwa kilometa 100 na kilometa 62.5 mkataba ulishasainiwa na kulikuwa na Lot I na Lot II. Lot zote mbili zilitangazwa mara moja. Swali langu la pili; je, hii Lot II kilometa 37.5 lini mkataba huu utasainiwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Lot I kilometa 62.5 imeshasainiwa na Mkandarasi tayari alishapatikana na kazi hii imeshainiwa. Kinachosubiriwa sasa hivi, Mkandarasi baada ya kusaini anatakiwa atoe performance guarantee (dhamana ya utendaji) na lazima iwe imetolewa ndani ya siku 28. Kwa hiyo, tunaamini atakapokuwa amekamilisha takwa hilo la kisheria atakabidhiwa hiyo barabara ili aanze kufanya mobilization na inatakiwa ifanyike ndani ya siku 28.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara hii ni kweli kama alivyosema ni kilometa 100 lot mbili, hizi kilometa 37.5 ambazo zimebaki, tayari kila kitu kimekamilika tunachosubiri ni kusaini tu, hii ni pamoja na barabara nyingine ambazo zilikuwa zinasubiria utaratibu wakuzisaini. Kwa hiyo, tunaandaa utaratibu ili barabara hizo ziweze kusainiwa halafu wakandarasi waanze kuzijenga. Ahsante. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa, barabara ya Mlowo – Kamsamba iliingizwa kwenye bajeti kwa mwaka huu wa bajeti tulionao. Ningependa kujua ni lini Serikali itaanza kufanya kazi kwa vitendo, kuwaona wakandarasi site? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara zote ambazo tumezitengea kuanza utekelezaji kwa mwaka wa fedha huu wa 2023/2024 ndiyo kwanza taratibu zinaandaliwa ikiwa ni pamoja na kuaanda tender documents ili ziweze kutangazwa, wakandarasi waombe na waweze kufanyiwa taratibu zote za manunuzi. Kwa hiyo, tupo kwenye taratibu za awali kwa sababu ndiyo tunaanza utekelezaji wa bajeti wa mwaka huu wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ziwa Nyasa ni karibu wiki moja limechafuka na akina mama wajawazito wameshindwa kabisa kuvuka kwenda kupata huduma pale Matema. Je, Waziri yuko tayari sasa kufuatana na mimi kuangalia jinsi gani barabara ya kutoka Matema kwenda Ikombe inavyosuasua?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tutoe pole kwa changamoto ambayo inatokea katika Jimbo la Kyela. Mheshimiwa Mbunge anafahamu kwamba yupo Mkandarasi ambaye alikuwa anasuasua na tayari tumeshamuagiza Meneja wa Mkoa wa Mbeya amsimamie ili kwanza aweze kukakamilisha eneo ambalo lilikuwa lina changamoto. Mimi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya hapa tukubaliane tuende tukatembelee ili kuhakikisha kwamba kazi ambayo inafanyika iweze kukamilika. Nipo tayari kufuatana naye.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mtwara – Pachani – Luchili – Mkungu – Mtwara Matata – Ligera – Ligunga – Lusewa – Magazine – Lingusenguse – Nalasi – Mbesa mpaka Tunduru ina urefu wa kilometa 305, barabara hii ni ya kimkakati. Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunatambua barabara hii ni kweli ni ya kimkakati na ya kiuchumi, tunachofanya sasa hivi, tulishakamilisha usanifu. Tulichoamua sasa hivi kutokana na urefu wa barabara na umuhimu wa hii barabara, tumeainisha maeneo yote ambayo yanasumbua pamoja na madaraja, tuyaimarishe na kujenga zege ama lami nyepesi ili barabara ile ipitike muda wote wakati huu tunatafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Kitonga ni barabara ambayo ni ya Kitaifa na imekuwa ikipitisha malori makubwa, inapopata ajali kidogo malori yamekuwa yakikwama kwa siku nzima au siku mbili, Serikali ilikuwa imetuahidi kujenga barabara mbadala ambayo itatokea Mahenge – Kudekwa kupita Wotalisoli mpaka Ilula.
Je, ni lini sasa ile ahadi ya Serikali itatekelezeka ili kuondoa changamoto kubwa katika Mlima Kitonga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tuna kazi mbili ambazo tunazifanya, moja ni kuendelea kuipanua ile barabara ili iwe pana hasa hilo eneo la Kitonga, kuruhusu magari yaweze kupishana na kunapotokea changamoto tupate nafasi ya magari mengine kupita.

Mheshimiwa Spika, suala la pili ni kweli Serikali ina mpango wa kujenga bypass (njia ya mchepuko) kuchepusha kupita huo Mlima Kitonga kunapotokea changamoto na tumeunganisha nguvu kati ya TANROADS na TARURA ambao wanaendelea na usanifu wa hiyo barabara, baada ya hapo hiyo barabara itajengwa, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa.

Je, Serikali ina mkakati gani kukamilisha barabara ya Kiboroloni – Kichudini mpaka Kidia, kwa sababu barabara hii itakuwa inapandisha watalii kupitia Lango la Kidia. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Kiboroloni sasa hivi inasimamiwa na TANROADS kupitia Meneja wa Mkoa na imepangiwa fedha ya maendeleo kwenda kwa awamu. Sasa pengine tutaangalia ukubwa wake ili kama inawezekana tuweze kuongeza fedha ili kipande kile kidogo kilichobaki kiweze kukamilika na ijengwe yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Mwezi wa Sita tulisaini barabara ya Mafinga – Mgololo kupitia ule utaratibu wa EPC+F. Sasa wananchi wanapata shaka, wanasema mbona hawaoni mkandarasi, naomba Mheshimiwa Naibu Waziri awape comfort wananchi wa Mafinga katika barabara hiyo inayo - cut across Majimbo Matatu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa miradi yote ya EPC+F Wakandarasi walishapatikana na walishasaini mikataba ikiwa ni pamoja na hiyo barabara ya Mafinga kwenda Mgololo. Kinachofanyika sasa hivi ni kwamba Wakandarasi wote wapo wanapita site, moja ikiwa ni kuangalia fidia, kuangalia sehemu watakazopata material, wapi watajenga kambi lakini pia hizi barabara kutokana na ukubwa wake kuzigawa kwenye lot kulingana na mazingira yake watakavyogawa Wakandarasi maana yake atakayejenga siyo Mkandarasi mmoja kulingana na ukubwa wa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna barabara ambazo zitakuwa na Wakandarasi wawili, hadi wanne kulingana na ukubwa. Kwa hiyo, Wakandarasi wako wanapita na kupitia pia usanifu kwa sababu ni wao pia wanatakiwa wajiridhishe na usanifu uliofanyika kabla ya kuanza ujenzi. Kwa hiyo, niwahakikishie wananchi kwamba mpango huo unaendelea na watu wapo kazini, kitakachofanyika baada ya kukamilisha wataanza kuona mitambo ikiwa inawasili kwenye maeneo yao, ahsante. (Makofi)
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Busisi – Sengerema hadi Igaka boarder ambayo inajengwa kwa barabara nne kwa kiwango cha lami. Lini kazi hiyo ya usanifu itaanza kufanyika maana yake toka imesemwa toka mwezi wa sita mpaka leo hatujamuona mkandarasi akifanya designing?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tukishafanya usanifu kinachofuata ni kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza huo ujenzi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa Serikali imeshatoa commitment kwanza kufanya usanifu, basi hatua inayofuata itakuwa ni kujenga hiyo barabara kama ilivyosanifiwa. Kwa hiyo, mpango huo upo, hela zikishapatikana tutaanza kuijenga hiyo Barabara. Ahsante.

MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Spika, barabara ya Bonyokwa – Kinyerezi walisema itaanza mwezi wa sita mpaka sasa hivi hajiaanza, je, ni lini itaanza hiyo barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba hiyo barabara tumeitengea bajeti kwenye bajeti ya mwaka huo wa 2023/2024 na kama nilivyosema kwenye barabara zingine ambazo zimepewa fedha kwa mwaka huu taratibu zipo zinaandaliwa ili zianze kujengwa ikiwa ni pamoja na hiyo barabara ya Bonyoka – Kinyerezi. Ahsante.
MHE. MARTHA N. GWAU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi. Kwa kuwa Mkoa wa Singida ni jirani kabisa na Mkoa wa Dodoma ambao ndiyo Makao Makuu ya nchi: Je, ni lini Kiwanja cha Ndege Singida kitakamilika ili wananchi wa Singida wapate huduma; lakini pia uwanja huo wa Singida utumike kama uwanja wa dharura kama Dodoma kuna changamoto? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Singida ni mkoa ambao uko karibu na Dodoma na Serikali tayari imeshafanya usanifu wa Uwanja wa Singida ili uweze kujengwa, kwani unaweza ukatumika sana pale ambapo kunatokea changamoto katika viwanja vya Mkoa wa Dodoma, ahsante. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi kwa kunisaidia. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya usanifu kukamilika, hatua inayofuata sasa ni kujua mahitaji halisi kwa ajili ya fidia ili hatimaye tuweze kuanza kufanyia kazi huo uwanja. (Makofi)
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; barabara ya Bungu kuelekea Kibirizi ambayo inamilikiwa na TANROADS hali yake ni mbaya sana na haipitiki kwa sasa. Je, mna mpango gani wa kukarabati barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, bahati nzuri barabara hiyo naifahamu sana, siyo barabara ndefu ni barabara ambayo ipo katikati ya Mji. Naomba nitumie nafasi hii kumuagiza Meneja wa TANROADS aipitie hiyo barabara na iweze kukarabatiwa kwa sababu imetengewa fedha kwenye matengenezo ya kawaida. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge barabara hiyo itakarabatiwa katika kipindi hiki cha mwaka wa fedha.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza Serikali Bunge lililopita iliahidi kujenga na kusaini barabara ya Bigwa – Kisaki hadi sasa ipo kimya; je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Bigwa – Kisaki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, barabara hiyo imeshapata mkandarasi na sasa hivi kinachoandaliwa tu ni taratibu za kuisaini hiyo barabara. Kwa hiyo tuna barabara kama 16 ambazo zinaandaliwa utaratibu mzuri wa kuzisaini ili Wakandarasi waanze kazi, ikiwepo na hiyo barabara ya Bigwa – Kisaki.

MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa barabara hii imeahidiwa toka Serikali ya Awamu ya Nne na iko kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi.

Je, ni lini Serikali sasa itatenga angalau kwa kilomita chache ili kuwezesha wananchi wale wa Bonde la Eyasi kuweza kusafirisha mazao yao kwenda kwenye masoko ya nchi ya jirani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na tunatambua kwamba barabara hii ni muhimu sana. Kama nilivyosema katika jibu la msingi, barabara hii ilitakiwa ijengwe lakini imejengwa barabara ambayo ni Serengeti Southern Bypass.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inachofikiria kufanya ni kujenga walau kilometa 50 ambazo zitaanzia pale Njia Panda hadi eneo la Mang’ola ambalo lina uzalishaji mkubwa sana na hasa zao la vitunguu. Kwa hiyo, Serikali sasa inafikiria kulifanya halafu baadae ndiyo ije kukamilisha kipande kilichobaki ambacho kinapita sehemu kubwa ya mbuga, ahsante.

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, hali ya Daraja la Mto Ubagwe hali ni mbaya sana na Mheshimiwa Waziri ni shahidi alituma watu wa TANROADS.

Ni lini Serikali inaanza ujenzi wa daraja hili ili kuwanusuru wananchi na hali ya mvua?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafahamu na tumefanya mawasiliano makubwa, nimtoe shaka naamini daraja hilo ambalo ni muhimu sana kwa Wilaya ya Ushetu litaanza kujengwa kipindi hiki cha mwaka huu wa fedha, ahsante.

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, pamoja na kutengewa fedha kwenye bajeti, bado hakuna hatua yoyote ambayo imeanza mpaka sasa.

Ni lini Serikali itaanza taratibu za ujenzi wa barabara ya lami ya kutoka Korogwe – Dindila – Soni mpaka Bumbuli? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii anayoitaja Mheshimiwa Mbunge tumeitengea bajeti, kwa maana ya utekelezaji wa mwaka huu wa fedha, tayari tender documents zinaendelea kuandaliwa ili barabara hiyo iweze kutangazwa kwa ajili ya kuanza ujenzi. (Makofi)
MHE. STANSALAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, kutokana na jibu la swali la msingi, kwamba tayari barabara hii imeshasainiwa mkataba. Naomba kuiuliza Serikali baada ya kusaini mkataba ni muda gani Mkandarasi huyu anaanza kujenga hiyo barabara ya Karatu – Haydom – Maswa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, pamoja na barabara nyingi ambazo ziko takribani sita, ziko kwenye EPC+F, baada ya kusaini nilijibu hapa kwamba, wakandarasi wameendelea kuoneshwa hayo maeneo na barabara hizi zinasimamiwa na makao makuu.

Mheshimiwa Spika, kinachofanyika sasa ikiwepo na hiyo barabara ambayo inapita kwenye Jimbo la Mheshimiwa Mbunge, ni kuwaonesha wakandarasi, wakandarasi kuzigawa zile barabara kwenye vipande (lots) zaidi ya nne na kutafuta wakandarasi wengine ambao watasimamiwa na huyo mkandarasi mkubwa kwa ajili ya kujenga hizo barabara. Kutakuwa na vipande visivyopungua vinne katika kila barabara, kwa maana ya makambi, kutafuta maeneo ambayo yana raw materials, kwa maana ya kokoto na changarawe, tayari wako wanapita na kujitambulisha kwenye hizo barabara. Kwa hiyo, mchakato unaendelea, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona; barabara ya Pachayamindu – Ngapa kuelekea Nachingwea, ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama, je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge, Serikali inatafuta fedha ili kwanza iweze kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, baada ya hapo gharama itajulikana na Serikali itafuta fedha kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, je, ni lini kipande cha barabara cha kuanzia Malagarasi – Mpeta mpaka Uvinza kitakamilishwa kujengwa kwa kiwango cha lami?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ni kusimamia utekelezaji, kwa sababu hicho kipande alichokitaja cha kilometa 51.3, Mkandarasi yuko site, tukisaidiana na mwenzetu wa Abu Dhabi. Kwa hiyo, ni suala tu la kuwasimamia kuhakikisha kwamba wanakwenda kwa kasi ili kiweze kukamilika, maana ndiyo kipande pekee kilichobaki cha vumbi kutoka hapa hadi Kigoma. (Makofi)
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Mpanda – Uvinza – Kasulu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge, barabara hii tumeshakamilisha usanifu na itakuwa ndiyo barabara kuu ya kutoka Kusini kwa maana ya Mpanda – Uvinza hadi Kasulu ambayo haizidi kilometa 57.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kweli inatafuta fedha ili iweze kukamilisha hicho kipande ambacho ndiyo kimebaki peke yake katika Mkoa wa Kigoma, barabara kuu ambayo haina lami. Kwa hiyo, tunalifahamu na Serikali imeendelea kutafuta fedha ili kukamilisha kipande hicho kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ninaomba kujua Mheshimiwa Naibu Waziri umepita sana barabara ya Sanzati kwenda Nata. Sasa ni lini hiyo barabara itamalizika maana imekuwa kero kwa wananchi wa Bunda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nichukue nafasi hii kusema kwamba, Mkandarasi tayari yuko site anafanya kazi. Nawahimiza Watendaji wa TANROADS pamoja na Meneja wa Mkoa ambao wanamsimamia Mkandarasi, kuhakikisha kwamba wanamsimamia ili aongeze kasi na kukamilisha barabara hiyo ambayo inahitajika sana kwa wananchi wa Bunda pia wananchi wa Wilaya ya Serengeti.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru, miradi ambayo itaendeshwa na the so-called EPC+F, ni programu ambayo ililetwa na Serikali hapa Bungeni, lakini majibu ya Waziri unavyojibu ni kama vile huna uhakika hizi barabara zitakamilika lini. Sasa unataka kutuambia wakati mnaandaa hiyo programu, mlikuwa hamjajua zile barabara mlizolenga changamoto zake zikoje, mahitaji yake yakoje na yatafanikiwa vipi? Maana majibu yako hayaeleweki.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imekuja na mpango huu uko kwenye bajeti na inajua itafanyaje, lakini mpango mpya kabisa katika nchi yetu. Kwa hiyo, kinachofanyika na ndiyo taratibu zake kwamba unakuwa na Mkandarasi mmoja katika kila barabara, mkandarasi mkubwa kwa sababu barabara ni ndefu, anakuwa na sub-contractors ambao ni lazima ajiridhishe na afanye tathmini pia ya kwake kwa sababu, yeye ndiye anayesimamia ujenzi wa zile barabara, kwa maana yote kwamba EPC (Engineering Procurement) na yeye ndiyo anayefanya pia procurement. Kwa hiyo, lazima baada ya kumkabidhi ile barabara ajiridhishe namna pia atakavyogawa hizo barabara.

Mheshimiwa Spika, kazi ya Serikali ni kumpa fedha na kazi hizo zinaendelea, walioko kwenye zile barabara sasa hivi wako wanaoneshwa zile barabara. Kwa hiyo, watakapoanza, watakuwa pia wamejiridhisha maana yake baada ya kukubaliana hakutakuwa na variation kwenye hizo barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kwanza ninashukuru kwa majibu mazuri yanayotia tumaini kutoka Serikalini. Vilevile ninashukuru kwenye ile barabara yangu ya Nachingwea – Liwale, tarehe 12 yule mkandarasi anaenda kukagua. Nashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hivyo, nina maswali mawili; barabara hii niliyoitaja inayounganisha Morogoro, tayari TANAPA wameshaanza kuichonga. Sasa tunachotaka kujua; je, sisi tunaweza kuanza kupita hata kabla ya huo upembuzi yakinifu na usanifu wa kina uliotajwa?

Swali la pili, tayari kwenye bajeti iliyopita tunayo barabara yetu ya Nangurukuru – Liwale kilometa 230. Tulishapewa kilometa 72 wananchi wa Liwale wanataka kujua ujenzi unaanza lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Liwale kwenda Mahenge ambayo inapita katikati ya Hifadhi ya Mwalimu Nyerere, tumetenga fedha kama nilivyosema. Kwa maana ya kutumika kwa sasa waliofanya hiyo barabara ni wenzetu wa Maliasili na Utalii kwa shughuli zao, lakini sisi kama Wizara tunapokwenda kuifanyia upembuzi yakinifu ni kwa maana ya wananchi waweze kutumia.

Mheshimiwa Spika, tuna hakika kama tutakavyokuwa tumefanya usanifu, wenzetu wa maliasili watashauri ijengwe vipi ili iweze kutumika kama barabara ya kiulinzi, pia, iweze kuwahudumia wananchi wote wa Tanzania bila kujali ni wa hifadhi ama siyo hifadhi, ndiyo maana Serikali imetoa fedha ili kurahisisha mawasiliano kati ya wananchi wa Liwale na Mahenge. Kwa hiyo, itaanza kutumika na wananchi kama itakuwa imekidhi hivyo vigezo.

Mheshimiwa Spika, suala la pili; ni kwamba, Barabara ya Nangurukuru – Liwale tumetenga tuanze ujenzi mwaka huu kilometa 72 kuanzia Liwale kwenda Nangurukuru. Ninataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tayari taratibu za manunuzi za awali zimeanza ili barabara hii ianze kujengwa. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nitumie nafasi hii kuishukuru sana Serikali ya Awamu ya Sita kutekeleza miradi yetu kwa haraka sana, lakini pamoja na hilo naomba niulize maswali au maombi mawili kwa Serikali.

Mheshimiwa Spika, moja, hapo ambapo tumewekewa kivuko cha pundamilia na taa sasa hivi tunavuka salama, lakini inatubidi tutembee mita sabini pembezoni mwa barabara ili tuingie kwa Musuguri ambapo jioni tunagongwa sana na magari. Ni ombi kwa Serikali, haioni sababu au haja ya kutengeneza Barabara ya wapita kwa miguu katikati ya road reserve ili tuweze kuingia kwa Musuguri kwa usalama?

Mheshimiwa Spika, pili, kwa chini hapa kwenye makutano ya Magari Saba na Mbezi kuna kivuko kingine ambacho Serikali imeanza kukijenga kwa kuweka taa, lakini imekiacha kwa muda mrefu. Je, ni lini Serikali itakamilisha taa zile ili nah apo wananchi wavuke kwa usalama?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa maswali mawili ya nyongeza na pongezi.

Mheshimiwa Spika, hili suala ni la utekelezaji. Naomba nichukue nafasi hii kumuagiza Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam pamoja na TANROADS Makao Makuu waende wakaone uwezekano wa haya mawazo ya Mheshimiwa Mbunge kuona namna watakavyofanya ili wananchi waweze kutumia haya maeneo ya road reserve ili waweze kupita kwa usalama katika eneo hili. Hili ni suala la utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, na suala la pili pia ni utekelezaji kwa sababu, mkandarasi yuko site, waweze kumsimamia na kuhakikisha kwamba, anakamilisha kazi ambayo anaendelea nayo ya kukamilisha mataa, ili kuweza kuleta usalama hapa katika hii barabara ya njia nane. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwenye swali hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inaunganisha Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Morogoro pia imekuwepo kwenye Ilani za Uchaguzi za CCM tangu enzi za Mzee Mkapa, Mzee Kikwete, Hayati Magufuli na sasa Rais Samia. Je, kwa nini Serikali isiweke Wakandarasi Mwaka wa Fedha 2023/2024 kwa barabara nzima kilometa 104 yaani Turiani – Mziha – Handeni badala ya kuweka kipande hicho kidogo? (Makofi)

Swali la pili la nyongeza, kwenye bajeti za Wizara hii kwa mwaka wa fedha 2020/2021, 2021/2022, 2022/2023 na sasa 2023/2024 barabara hii imekuwa ikitengewa kiasi hiki cha fedha cha bilioni moja na majibu ya Serikali yamekuwa ni haya haya.

Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Mkoa wa Tanga na Mkoa wa Morogoro kuhusu barabara hii na ahadi zake zisizotekelezeka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli barabara aliyoitaja ipo kwenye Ilani na ni kweli kwamba inaunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Tanga, ni barabara ambayo kwa kweli ina historia yake na kwa maana hiyo Serikali ilishaanza kuijenga hadi Turiani, kwa sasa Serikali imedhamiria kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kuanzia Turiani, Mziha hadi Handeni, Kilometa 104, lakini kuweka Wakandarasi zaidi ya mmoja utaharakisha lakini kutategemea sana na upatikani wa fedha ili kuweza kuweka Wakandarasi zaidi ya mmoja kwa kipindi kimoja. Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwamba kwa mwaka ujao wa fedha tunaendelea pale tulipoishia kukamilisha barabara hii hadi Handeni. Ahsante. (Makofi)
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona.

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa barabara ya Katoma hadi Bukoli kwa kiwango cha lami ndani ya Wilaya ya Misenyi, Mkoani Kagera?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Semuguruka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Katoma kwenda Bukoli ipo inaendelea kujengwa lakini kwa awamu. Mwaka huu wa fedha imetengewa pia fedha ambapo tunategemea kwamba tutajenga zaidi ya kile tulichokuwa tunakijenga ili kuikamilisha barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itasaini mkataba wa ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami, barabara kuanzia Kongwa – Kiteto – Simanjiro hadi Arusha na Tanga – Kiteto hadi Singida? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti tulitaja barabara aliyoitaja Kongwa - Kibaya – Orkesumet - Losinyai hadi Arusha ambayo tunachosubiri sasa ni baada tu ya Bunge hili sasa ambalo tunategemea kabla ya Mwezi Juni barabara hiyo iwe imesainiwa kwa mpango wa EPC + F. Ahsante. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Masasi – Nachingwea - Liwale itajengwa kwa utaratibu wa EPC + F tuliambiwa Mkandarasi amepatikana. Ni lini mkataba utatiwa saini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kama nilivyojibu katika swali ambalo nimeulizwa barabara hizi ziko saba na moja ya barabara hiyo ni ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale. Mikataba ilishakamilika kinachosubiriwa ni muda na kwa sasa kwa sababu ni miradi mikubwa signing itafanyika muda wowote iko tayari kwa ajili ya signing na tunategemea kabla ya mwisho wa mwezi Juni barabara hii ya Masasi – Liwale – Nachingwea kilometa 175 itakuwa imesainiwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Barabara ya Utegi – Shirati mpaka Kirongwe kwa kuwa upembuzi yakinifu umekwishakamilika na barabara imeingizwa kwenye bajeti. Nataka nijue nini mpango wa Serikali sasa kuanza ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ndiyo imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi, tunajua upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishakamilika, kwa hiyo taratibu za manunuzi kuanza ujenzi wa barabara hiyo zitaanza mwaka wa fedha wa 2023/2024 kama ilivyopitishwa na Bunge hili kwa maana ya mwaka ujao wa fedha. Ahsante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itahakikisha alama zote muhimu katika barabara kuu za nchi yetu zinawekwa na zinasomeka vizuri?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara zote zinazojengwa kisheria ni lazima ziwekewe alama zote za barabarani kwa sababu hizo ndizo zinazoongoza watembea kwa miguu, lakini pia wanaotumia magari na vyombo vyote vya moto, na kila tunapojenga barabara hizo kwa kweli huwa tunajitahidi kuweka alama.

Mheshimiwa Spika, changamoto ni kwamba kuna maeneo ambayo tukishaweka hizo alama, na hasa zile za vyuma inatokea baadhi ya wananchi huziharibu, hiyo ndiyo changamoto. Lakini pengine nitumie nafasi hii kuwaomba wananchi kwamba alama zote za barabarani zina umuhimu sana kwa maisha yetu na wale watumia barabara zetu muda wote.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nitoe shukrani za dhati sana kwa Serikali yetu kwa kutujengea daraja hili ambalo lilikuwa linaleta usumbufu mkubwa sana kipindi cha mvua. Baada ya shukrani hizo, sasa nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata hizi mbili za Songwe na Bokwa kuna ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami; je, Serikali iko tayari kuweka taa katika eneo hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kuna Madaraja mawili ya Chakwale na Nguyami ambayo yanunganisha Wilaya za Kilindi na Gairo. Je, ni lini Serikali itajenga madaraja hayo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Kilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sasa barabara zote zinazojengwa na zinazopita kwenye miji mikubwa ama centers kubwa, maelekezo ni kwamba ni lazima tuweke taa kwa ajili ya matumizi ya usiku katika miji yote ambayo ni mikubwa. Kwa hiyo kwa barabara hiyo ambayo inajengwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tathmini itafanyika na tutahakikisha kwamba tunaweka taa.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali lake la pili, tumeshakamilisha usanifu wa kina mwaka huu wa fedha kwa Madaraja yote mawili ya Chakwale na Nguyami ambayo yanaunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Tanga, na tumepanga fedha, kwamba mwaka 2023/2024, Madaraja yote hayo mawili ya Chakwale na Nguyami yanakwenda kuanza kujengwa, ahsante. (Makofi)
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza maswali ya nyongeza:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi ya Awamu ya Sita kwa kuiona barabara ile kwa kuwa imekuwa na changamoto kubwa sana. Naishukuru Serikali kwa kuingia mkataba wa kutengeneza barabara ile ya Mkomazi – Kisiwani – Same. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja tu la nyongeza. Kuna maeneo ambayo yalitengenezwa kwa kiwango cha lami, kilometa tano, tatu na tano tena; katika Kata ya Ndungu zimetengenezwa kilometa tano, katika Kata ya Maore zimetengenezwa kilometa tano na katika Kata ya Kihurio zimetengenezwa pia kilometa tano…

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa.

MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Je, Serikali sasa kupitia mkataba huu itabomoa ile lami ambayo imetengenezwa ambayo imeanza kuchakaa au itaendelea na ile ile? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Zuena Bushiri, Mbunge, Viti Maalum, Mkoa wa Kilimanjaro, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza napokea hizo pongezi kwa niaba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kuhusu suala lake la maeneo ambayo tumeyajenga, wakati hizi barabara zinajengwa kwa vipande vipande yalikuwa ni maelekezo kutokana na wananchi wa maeneo hayo yalivyokuwa korofi, lakini pia kwenye miji midogo waliomba viongozi na wakatoa maelekezo barabara hizo ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami kwa vipande vipande.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba pamoja na wananchi ambao wanahusika na hiyo barabara, usanifu uliofanyika, hayo maeneo yameshakuwa yamechakaa na hayaendani na usanifu wa sasa. Kwa hiyo, maeneo yote yale yatafumuliwa na yatajengwa upya, isipokuwa kuna kilometa tano na kitu ambayo inaendela kujengwa, hiyo ndiyo ianendana na usanifu wa sasa, lakini maeneo yote ya zamani yatafumuliwa na kujengwa upya, ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni lini Barabara ya Tengeru – Holili itaanza kupanuliwa ikiwa ni pamoja na kujenga daraja jipya la Kikavu?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja pamoja na daraja hilo, tayari yapo mazungumzo, na JICA wameshakubali kufadhili ujenzi wa barabara hiyo na daraja hilo la Kikavu ikiwa ni pamoja na barabara kama kilometa 10 katika Mji wa Moshi. Kwa hiyo, sasa hivi suala linaloendelea ni mazungumzo kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na JICA ili tuanze kujenga hayo maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge, ahsante. (Makofi)

MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Barabara ya Mkomazi – Kisiwani – Same ni kweli ina madaraja mengi sana: Je, Mheshimiwa Waziri, Daraja la Saseni na Daraja la Mpirani, nayo mtayarudisha yawe mapya kama ambavyo barabara itakuwa mpya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Same Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, usanifu huu ni mpya tofauti na uliokuwepo zamani. Kwa hiyo kila kitakachofanyika ni kujenga barabara yote, hizo kilometa 98 ikiwa ni pamoja na hayo madaraja, ahsante. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Mbalizi – Shigamba, ile barabara ni muhimu sana, ambayo inaunganisha na Mkoa wa Songwe;

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hiyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hili swali linajirudiarudia lakini halijapata majibu sahihi ya Serikali; barabara ya kutoka Katumba – Suma – Mwakaleli – Luangwa – Mbambo na Tukuyu Mjini, hii ni ahadi ya tangu awamu ya nne;

Je, ni lini Serikali itaanza kuijenga barabara hiyo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbalizi – Shigamba tayari tulishapata maelekezo na tunaifanyia kazi. Hivi sasa tunakamilisha usanifu wa kina na mhandisi mshauri yupo kazini. Akishakamilisha barabara hii ambayo ni ya Mbalizi – Shigamba na inaunganisha Itumba na Malawi, sasa Serikali itaanza kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, na barabara ya pili aliyoitaja, kimsingi tumeshaitengea fedha kwa kipande kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Njombe – Mdandu – Iyai kutokea Mbeya kwa kuwa barabara hii ni muhimu ndani ya Jimbo la Wanging’ombe na hatuna barabara ya lami yoyote zaidi ya hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema William Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara inayoanzia Njombe – Ramadhani – Iyai, Serikali imekuwa inajenga kwa awamu. Na katika mwaka huu wa fedha nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tumetenga fedha kwa ajili ya kuendelea kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami kuunganisha Makao Makuu ya Wanging’ombe na Makao Makuu ya Mkoa wa Njombe.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Napenda kuuliza Serikali ina mpango gani wa kuifanyia matengenezo barabara ya ulinzi ya Kusini sehemu ya Kivava – Kitaya baada ya mafuriko yaliyotokea hivi karibuni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja ya vipaumbele vya Serikali ni kuhakikisha kwamba barabara zote za ulinzi zinapitika. Barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge bado ni barabara ya changarawe, na kutokana na mvua iliyonyesha kama alivyosema, kuna maeneo ambayo hayapitiki.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tayari imeshaanza kufanya mipango ya kurudisha mawasiliano maeneo yote yaliyokatika ili iweze kupitika, hasa tukizingatia umuhimu wa barabara yenyewe, barabara ya ulinzi, ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Bukonyo – Bukongo – Masonga yenye kilometa 32 kwa sababu upembuzi yakinifu ulikwisha fanyika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Ntengo Matondo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge itajengwa baada ya kufanya usanifu wa kina wa mwisho ambapo ile barabara bado hatujafanya usanifu. Kwa hiyo tukishafanya usanifu tutajua gharama na ndipo Serikali sasa itatafuta fedha kujenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Namanyere – Kipili Port ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Wilaya ya Nkasi na Mkoa wa Rukwa kwa ujumla;

Je, ni lini barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama alivyosema Mbunge barabara hii inakwenda kwenye Bandari ya Kipili. Tumetenga fedha kiasi kwa ajili ya kuifanyia ukarabati mkubwa ili iweze kupitika. Lakini lengo la Serikali ni kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami, hasa tukizingatia umuhimu wenyewe, kwamba inakwenda kwenye bandari ambayo inahusisha biashara kati ya Tanzania na DR Congo. Ahsante.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani nyingi kwa Serikali kwa kukamilisha kipande cha Lusitu - Mawengi na kuanza kipande cha Itoni – Lusitu ambapo kipande kile cha mwanzo kilitumia bilioni 179 cha pili bilioni 90 bado ninaomba kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza, pale Mawengi wakati wanajenga ile barabara kuna wananchi wachache ambao hawakulipwa fidia wamekuwa wakihangaika sana;

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi wale ili waache kuhangaika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ningepena kufahamu Serikali imejenga barabara nyingi Ludewa lakini haijaweka taa za barabarani;

Je, ni lini Serikali itakwenda kuweka taa za barabarani hasa maeneo yenye miji ambayo yana wananchi, ili mji wetu uweze kuonekana wa kisasa zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kamonga Mbunge wa Ludewa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu fidia; wananchi hawa ni kweli walikuwa hawajalipwa na ni kwa sababu zoezi wakati la ulipaji linaendelea hawa wananchi hawakuwepo. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge na wananchi hao waweze kumuona Meneja wa Mkoa wa Njombe ili aweze kuwapa taratibu zitakazofanyika namna ya kuwalipa wananchi hawa ambao walipisha ujenzi wakati wa mradi huu, hawa wananchi wa Mawengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kuhusu taa za barabarani. Kama tulivyosema sehemu zote za wilayani na kwenye miji ama center kubwa ni mpango sasa wa Serikali kuhakikisha kwamba tunaweka taa za barabarani. Na katika mwaka wa fedha ujao nataka nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge moja ya eneo ambalo litafaidika kuwekewa taa ni pamoja na mji wa Ludewa, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kukamilisha barabara ya Kibosho Shine hadi kwa Rafael kwa kiwango cha lami?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Prof. Ndakidemi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya Kibosho Shine kwenda kwa Rafael ina hudumiwa na Wakala wa Barabara Tanzania lakini kuna kipande ambacho pia kinahudumiwa na wenzetu wa TARURA. Kwa upande wa barabara ambayo kwa sasa inahudumiwa na TANROADS ni mpango wetu kuhakikisha kwamba tunaijenga yote kwa kiwangio cha lami, na hadi sasa mkandarasi yuko site. Na katika mwaka unaokuja pia tumetenga fedha kuendelea na ujenzi kwa awamu kwa kiwango cha lami ili kuikamilisha barabara yote hiyo kuijenga kwa kiwango cha lami.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza;

Je, lini Serikali itakamilisha barabara ya kutoka Mji Mwema mpaka Pemba Mnazi ni ya muda mrefu sana?

Je, lini sasa itakamilisha kipande cha kutoka Gomvu mpaka Pemba Mnazi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, nataka kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilishafanya taratibu na tuko kwenye hatua za manunuzi kwa maana ya kujenga barabara ya kilometa 41 kwa kiwango cha lami. Barabara ambayo ametaja kilometa 41.
MHE. MWITA W. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara inaunganisha Wilaya ya Tarime na Wilaya ya Serengeti na ndiyo barabara ya kwanza ya lami katika Jimbo la Tarime Vijijini. Tunampongeza Mheshimiwa Rais kupeleka fedha hapa kujenga barabara hii. Lakini kwa majibu ya Serikali barabara hii imefika asilimia 15, na tumeambiwa Tarehe 24 Mwezi wa Januari Mwaka kesho tunakabidhiwa barabara ya lami. Lakini mkandarasi alipeleka certificate Serikalini Oktoba 2022 akidai milioni 874, hajalipwa. Akapeleka certificate ya pili Machi 2023 akidai milioni 841, hajalipwa. Certificate ya tatu ni Mwezi wa tatu mwaka huu ambayo ni bilioni 1.6.

Je, ni lini, Serikali italipa fedha hizi ili tupate barabara ile Januari mwakani kutengeneza kura za Chama Cha Mapinduzi katika jimbo langu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Barabara hii ina center ya Mogabiri, center ya Nyamwigora, center ya Kimakolele, center ya Nyarero, center ya Kiwanja, center ya Gena na kule Nyamongo;

Je, maeneo haya tutawekewa taa za barabarani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na swali la pili la Mheshimiwa Mbunge swali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema katika barabara hii ya Tarime – Nyamwaga – Nyamongo hadi Mugumu, tumeainisha maeneo sita ambayo yatawekwa taa. Yale maeneo yote, vijiji vyote vile vikubwa, maeneo sita yatawekewa taa na Mheshimiwa Mbunge pengine baada ya hapa anaweza kuja nimwoneshe vijiji ambavyo vitawekewa taa katika hiyo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ujenzi unaoendelea, mkandarasi bado yupo site anaendelea kujenga na tuna hakika changamoto iliyokuwepo kubwa ya barabara hii ni mvua kubwa inayoendelea kunyesha. Sasa Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba, kasi ya ujenzi itaendelea na hasa kwa kuwa Serikali sasa tumeshajipanga kuhakikisha kwamba, changamoto zilizokuwepo za malipo yote tunakamilisha na mkandarasi ataendelea na ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kipande kilichobaki tunategemea ikiwezekana kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha tutakuwa tumesaini mkataba kwa ajili ya barabara nzima hiyo ya Tarime – Nyamwaga hadi Mugumu. Ahsante. (Makofi)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza. Barabara ya Tegeta – Basihaya – Bunju mpaka Bagamoyo katika Jimbo la Kawe imejengwa bila mitaro ya maji. Kwa sababu hiyo, husababisha mafuriko makubwa sana kwenye maeneo ya Nyaishozi, Tegeta, Nyamachabes. Sasa, ni lini Serikali itajenga mitaro ya maji kuepusha hatari kwa wananci kwa sababu ya mvua zinazoendelea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Askofu Gwajima, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tunatambua katika kipindi hiki mvua imeendelea kubwa sana kwa Jiji la Dar-es-Salaam na eneo alilolitaja kwa kweli limeathirika kwa kiasi kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo aliyoyataja yote ya Basihaya, Msikitini, DAWASA na Nyaishozi yalikuwa yamefanyiwa design yaanze kujengwa kabla, lakini kwa kuwa tuna Mradi mkubwa wa BRT IV maeneo haya yatakuwa ni sehemu ya ujenzi wa Mradi huo wa BRT IV.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Jimbo la Kawe, tulichokifanya, tutawahusisha na tumehusisha pia TARURA ili wakati wa kujenga pia hiyo mitaro na wenzetu wa TARURA tusije tukajenga halafu kuwe na changamoto kwenye barabara zetu, kwa hiyo nao watahusika. Mkataba uko tayari kusainiwa. Kwa hiyo, muda wowote kazi ya ujenzi kwa BRT IV itaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini? Inawezekana hata ikawa Juni tukasaini huo mkataba. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ni lini mtapandisha hadhi barabara ya Uchira – Kisomachi - Kolarie?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge, kuhusu kupandisha hadhi hizi Barabara, kuna taratibu zake, ambapo kama Mheshimiwa Mbunge pamoja na vikao vya kuanzia wilaya, mkoa wataleta maombi, Wizara ya Ujenzi ambayo watakwenda kufanya tathmini na baada ya hapo kama itakidhi vigezo, maana yake ni kwamba hiyo barabara itakuwa imepandishwa hadhi. Pia kama itakuwa barabara hiyo haikupandishwa hadhi, wanaweza kuomba kukasimiwa kukarabatiwa ama kusimamiwa na TANROADS, ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Barabara ya Kigamboni mpaka Kongowe eneo la Mikwambe lina tatizo ya mifereji: Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga mifereji katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja, siyo tu mifereji, bali pia ni barabara ambayo kuna vipande vingi ambavyo vimechoka sana. Kwa hiyo, mpango wa Serikali pamoja na kutengeneza mifereji, pia ni kukarabati yale maeneo yote ambayo yamechakaa sana, ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hiyo. Barabara ya Kolandoto kwenda Kishapu ina kero kubwa kwa wasafiri na wasafirishaji. Ni lini Serikali itaanza kutekeleza mradi huu katika kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Kolandoto - Kishapu – Lalago, ni moja ya barabara kuu na Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba katika mpango huu wa fedha kwa maana ya bajeti ambayo tumepitishiwa, tayari tumeshatenga fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. NORAH W. MZERU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii; je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati barabara ya kutoka Nanenane – Tungi kupita VETA kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na utaratibu wa kufanya matengenezo ya barabara zote kwa kiwango cha lami, kwa hiyo hata mwaka unaokuja wa fedha tumetenga kwa ajili ya kukarabati maeneo yote ambayo yameharibika ili kuhakikisha kwamba barabara inarudi kwenye ubora wake. Ahsante.


MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kuna changamoto kubwa sana ya mlundikano wa malori ndani ya Mji wa Tunduma ambao unasinyaza na kufubaza uchumi wa Wana-Tunduma. Serikali mna mpango gani wa kujenga njia ya dharura ili kunusuru hali iliyopo kwenye Mji wa Tunduma? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kuna msongamano mkubwa sana katika Mji wa Tunduma ambao ndipo tunapotoka pale kwenda Zambia. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Tunduma kwamba tunakwenda siyo tu kufanya mpango wa dharura, lakini mpango kamili wa kujenga barabara ya njia nne katika Mji wa Tunduma ambapo tutakwenda kujenga kwa mpango wa EPC+F.

Mheshimiwa Spika, moja ya maeneo ambayo tunategemea kuanza ni pamoja na miji ya Tunduma ili kukwamua na kuondoa changamoto ambayo ipo inayosababisha msongamano mkubwa katika Mji wa Tunduma. Kwa hiyo, mkataba huo tunategemea utasainiwa Juni mwaka huu wa fedha, ahsante. (Makofi)
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya Makanya – Ruvu ambayo inakwenda kwenye machimbo ya gypsum? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni barabara ya kimkakati ambayo inaenda kwenye maeneo muhimu ya kiuchumi. Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ningependa kujua ni lini barabara ya kiusalama kutoka Susuni – Mwema - Sirari – Mriba – Nyamongo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami mara tu tutakapokuwa tumekamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa, barabara hii inahudumia mikoa mitatu Arusha, Manyara na Dodoma. Je, Serikali haioni sasa ni muhimu kuharakisha barabara hii ili kujenga uchumi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, kwa kuwa barabara hii iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025, Serikali haioni kutoharakisha barabara hii ni kutotekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika jibu la msingi, ni kweli barabara hii iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini pia ni kweli inaunganisha Mikoa mitatu, kwa maana hiyo ndiyo maana katika jibu langu la msingi hii barabara imetengewa fedha na tumeipitisha inaanza kujengwa kwa EPC+F na kama nilivyosema tutaisaini kuanza ujenzi wa barabara hii kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha kwa mwaka huu, kwa maana ya huu mwezi Juni. Ahsante. (Makofi)

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Je, Serikali haioni kwamba ni busara kukamilisha barabara ya Kilosa kwenda Mikumi ili kuongeza tija kwenye uwekezaji mkubwa wa reli ya SGR pale Kilosa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge wa Mikumi, siyo tu busara, lakini kwa kweli ni barabara ambayo ni muhimu, ambayo sasa itakuwa inaunganisha barabara ambayo tunaijenga kwa EPC kuanzia Namtumbo – Malinyi – Mikumi ambayo tunaona busara badala mtu kwenda Morogoro, itoke Mikumi kuja Kilosa. Kwa hiyo, hiyo mipango ipo kuhakikisha kwamba tunapafungua kati ya Kilosa na kuunganisha na Mikumi, ahsante.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara inayoanzia Nanganga kwenda Ruangwa inajengwa sasa kwa kiwango cha lami. Hata hivyo, wakazi wa Nanganga wanadai fidia. Ni lini Serikali italipa fidia kwa watu waliobomolewa nyumba zao eneo la Nanganga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:_

Mheshimiwa Spika, tumekuwa na utaratibu wa kulipa fidia tunapoanza ujenzi wa barabara zote. Namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama kuna changamoto kwa hiyo barabara, tuweze kuonana ili tujue tatizo ni nini ambapo wananchi hao wanaodai mpaka sasa hivi wakati barabara inajengwa na tulitatue kwa kuwalipa fidia hao wananchi wa barabara ya Nanganga hadi Ruangwa, ahsante.

MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga barabara ya Haydom -Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara ya Mogitu - Haydom ni barabara ambayo ni link kwenye ile barabara ya Karatu - Mbulu – Haydom kwenda Lalago. Kwa hiyo, ni link ya hiyo barabara. Kwa hiyo, ni sehemu ya hiyo barabara, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kujenga kilometa kumi za lami kwenye mitaa ya Mji wa Bunda?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kwa kushirikiana na wenzetu wa TAMISEMI, ipo mipango ya kutimiza hiyo ahadi ya kujenga barabara ya kilometa kumi ambazo ziliahidiwa na viongozi wetu katika Mji wa Bunda kwa kiwango cha lami. Ahsante.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Barabara ya Mbuguni kwa kiwango cha lami ambayo inaanzia Tengeru hadi Mererani?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge, ni ya kimkakati ambayo inakwenda machimbo ya Tanzanite. Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi kwamba mpaka sasa hivi tunaendelea kukamilisha usanifu wa kina na baada ya hapo Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga sasa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ASKF. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kwamba barabara ya kutoka Bunju B mpaka Mabwepande ijengwe kwa kiwango cha lami katika Jimbo la Kawe: Ni lini Serikali itatimiza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ya Bunju B – Mabwepande – Magohe – Mapigi hadi Kibamba, ni moja ya barabara ambayo sasa hivi inafanyiwa usanifu. Siyo tu ahadi ya viongozi, lakini tunategemea ndiyo itakuwa altering ya barabara za Mji wa Dar es Salaam. Kwa hiyo, ipo kwenye mpango na tunavyoongea sasa hivi Washauri Wahandisi wako kazini wanafanya usanifu, ahsante.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali: Je, mko yatari kuanza sasa usanifu na ujenzi wa barabara hiyo kwenye bajeti ya mwaka huu unaokuja Julai, 2023/2024?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika jibu langu la msingi, nilisema tunakamilisha usanifu wa kina mwezi huu tarehe 30 Juni. Tayari bajeti imeshapitishwa. Kwa hiyo, hiyo barabara itaingizwa kwenye mpango wa mwaka unaofuata kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyonyeza. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kuanzia Gairo – Chanjale - Kibakwe hadi Mpwapwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ishengoma kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hii barabara ilifanyiwa usanifu wa awali na bado haijafanyiwa usanifu wa kina. Kwa hiyo, barabara hii ikishafanyiwa usanifu wa kina, Serikali itakuwa imefahamu gharama ya hiyo barabara na ndiyo tutaanza sasa kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Barabara ya Bungu - Nyamisaki ni barabara ya muda mrefu sana kabla hata bandari haijajengwa. Tumeuliza haya maswali humu muda mrefu na siku nyingi na kila tukiuliza wanasema tutajenga. Tunaomba commitment ya Serikali, barabara hii mtaijenga lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salma Kikwete Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni ya siku nyingi na tunatambua umuhimu wake kwamba barabara hii ndiyo inayounganisha Pwani na Kisiwa cha Mafia. Commitment ya Serikali kama nilivyosema, ndiyo maana sasa tumeamua kuifanyia usanifu yakiwa ni maandalizi kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, tunavyoongea, kazi inaendelea. Kwa hiyo, tuna hakika baada ya kukamilisha usanifu, barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya kutoka Ifakara – Lumemo – Michenga – Idete mpaka Mlimba imeshatangazwa; je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante ni kweli kwamba barabara hiyo imeshatangazwa na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajenga kilometa 100 na tuna lots mbili. Kinachosubiriwa sasa hivi ni kusaini mikataba na wakandarasi ambao wamepatikana kwa ajili ya kuanza ujenzi huo wa barabara, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Barabara ya Nyoni - Maguu inayopitia Mawono kwenye mlima mkali, ni lini tutaanza ujenzi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Barabara anayoitaja Mheshimiwa Kapinga ni kweli, na ipo kwenye ilani kwamba ijengwe kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga, lakini kitu ambacho tunategemea tukifanye kwanza ni kuhakikisha kwamba yale maeneo yote yenye miinuko tunajenga aidha kwa zege ama kwa lami nyepesi ili kupunguza changamoto kwa wasafiri ambao wanasafiri katika hiyo barabara ya Nyoni – Maguu, ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Swali langu la kwanza la nyongeza, napenda kujua, ni lini Serikali itakarabati kipande cha barabara toka Somanga hadi Nangurukuru hadi Mbwemkuru ambacho kimechakaa sana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; miaka ya hivi karibuni Serikali ilitanua barabara za mikoa na barabara kuu katika Mkoa wa Lindi, lakini haijaweza kulipa fidia hadi wakati huu. Ni lini Serikali italipa fidia kwa wananchi walio kando kando ya barabara hizo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii kuu ya Kusini Somanga - Nangurukuru hadi Mbwenkulu hadi Mnazi Mmoja imechoka. Hii barabara sasa hivi inapitisha mizigo mizito sana tofauti na ilivyokuwa awali. Kwa hatua za haraka ni kukarabati yale maeneo yote ambayo yamechakaa sana ili kuhakikisha kwamba hatukwamishi magari. Mpango mkubwa wa sasa hivi, Serikali inatafuta fedha ili kuifanyia ukarabati wa barabara yote kuendana sasa na uzito wa magari ambayo yanapita kwenye hiyo barabara ya Kusini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili la Mheshimiwa Mbunge, ni kweli kwamba tulibadilisha sheria kwa maana ya kuongeza upana wa barabara. Wizara ya Ujenzi inachofanya sasa hivi ni kufanya tathmini kwa barabara zote. Kwa kuanzia, pale ambapo tunaanza ujenzi, tunalipa, lakini tunataka tupate gharama nzima kwa barabara zote ambazo zimeongezeka kwa ajili ya kutafuta fedha kuwafidia wananchi ambao barabara imewafuata, na siyo kwa Lindi tu, ni kwa sehemu kubwa ya nchi, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kipande hicho cha Mbagala Rangi Tatu hadi Kongowe kinakuwa na msongamano mkubwa wa magari kiasi kwamba ni foleni masaa yote: Je, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi kuhakikisha wanapanua ile barabara ili magari yaweze kupita na kuepukana na foleni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, tunatambua changamoto ambayo ipo kwenye hii barabara na ndiyo maana tumeiweka kwenye mpango. Serikali itakachofanya ni kuhakikisha kwamba inaanza haraka ujenzi wa kipande hiki ili kuondoa adha ambayo inawakuta wananchi ambao wanatumia hii barabara ikiwa ni pamoja na kupunguza msongamano kwa maana ya kupunguza muda mwingi ambao unatumika katika kipande hiki. Ndiyo maana tayari tumeshaingiza kwenye mpango. Kwa hiyo, cha msingi ni kuanza haraka ujenzi wa barabara hii kwa hizo njia nne, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kuwa barabara ya kuingia Singida Mjini, almaarufu kama barabara ya Kibaoni, imekuwa finyu: Ni lini Serikali itaitanua barabara hiyo na kuwa njia nne?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kinachofanyika ni study ya miji yote ambayo inaendelea kukua na Singida ikiwa mojawapo. Kwa hiyo, tunaendelea kufanya study kwenye miji mbalimbali ambayo tunaona kunahitajika kupanuliwa kwa barabara hasa zinazoingia kwenye miji. Hii ni pamoja na miji kama hii ya Dodoma, Singida ambayo tunaona kadiri kunapokucha magari yanaongezeka.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na usanifu wa hizo barabara ili tuone kama zinahitajika njia nne, ama njia sita, ahsante. (Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kuna wananchi wengi wa Mwibara uliopisha mradi wa barabara kati ya Bulamba na Kisorya imechukua muda mrefu kweli bila kulipwa. Sasa naomba commitment ya Serikali: Ni lini wananchi hawa watalipwa fidia zao?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu wakati najibu muuliza swali la msingi wananchi ambao bado hawafidiwa ni wale ambao wako kilomita I mean wako mita 7.5 kutoka kwenye barabara na ndiyo maana nilisema tunafanya tathimini ya nchi nzima. Wamepewa kazi hiyo wale Mameneja wa Mikoa kuangalia na kufanya tathimini ili tupate gharama halisi ili wakati Serikali inalipa basi iweze kujua gharama halisi ya fidia ambayo inatakiwa kulipwa ikiwa ni pamoja na wananchi wa Mwibara ambao wamepisha barabara hiyo ya Kisorya ya Bulamba, ahsante. (Makofi)

MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali. Napenda kusema tunashukuru sana Serikali hata kwa hicho cha kuanza na ukarabati wa barabara kutoka Songea mpaka Lutukila. Hata hivyo ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza, barabara hii ni mbaya sana, ni barabara kubwa ya kiuchumi na kuna shughuli nyingi sana sasa hivi. Sasa Serikali, wakati fedha zinatafutwa, hawaoni kwamba kuna umuhimu wa angalau kutenga fedha za kutosha ili maeneo ambayo ni hatarishi kwa magari mengi ya mkaa yaweze kuanza kushughulikiwa kwenye kona kali na miteremko?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Barabara hii ilifanyiwa redesign 2012, wakati huo Njombe haikuwa mkoa. Mji wa Njombe ambapo barabara hiyo inapita umebadilika, unakua kwa kasi, umekuwa na activities nyingi. Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri anaweza kutoa maelekezo kwamba sasa wafanye redesign pale katikati ya mji kutoka Kibena mpaka kufika Nundu ili paendane na uhalisia wa Mji wa Njombe ambao unaenda kuwa Manispaa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni utaratibu ambao umezoeleka kwamba katika hizi barabara kubwa, na hasa barabara aliyoitaja ni ya zamani, tumeendelea na tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati maeneo yale yote ambayo yanakuwa yamechakaa sana ili kuhakikisha kwamba wanaosafiri na wasafirishaji hawapati changamoto. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi huo Mheshimiwa Mbunge, Serikali itaendelea kukarabati yale maeneo yote korofi katika hiyo barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, ni kweli kama alivyosema, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Njombe ni mji unaokua sana kama mji na unapitisha magari mengi makubwa. Sisi kama Wizara tunataka tumhakikishie kwamba tutafanya redesign. Itakuwa ni dual carriageway katika Mji wa Njombe kuanzia Kibena Hospitali hadi Hagafilo na zitakuwa ni njia nne ili kuhakikisha kwamba hakutokei changamoto ya msongamano katika Mji wa Njombe, ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kufahamu Serikali imefikia hatua gani katika maandalizi ya kuijenga barabara ya Kondoa – Gisambalang – Nangwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Barabara ambayo ameitaja kwa kweli mpango mkubwa hasa ni kuhakikisha kwamba kuna daraja kubwa ambalo linaleta changamoto kati ya Kondoa na Hanang. Tunachofanya sasa hivi, kwanza ni kufanya usanifu wa lile daraja, tulijenge, halafu tuimarishe hiyo barabara ili iweze kupitika kipindi chote cha mwaka. Sasa hivi kwa kweli inapotokea masika hiyo barabara haipitiki, ahsante.
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza. Kwanza tunaishukuru Serikali kwa kutenga fedha za ujenzi wa meli mbili kwenye Ziwa Tanganyika, lakini mwaka 2022 Serikali ilitenga fedha, na mwaka huu Serikali imetenga fedha, lakini majadiliano bado yanaendelea: Je, nini mkakati wa Serikali wa kuharakisha ujenzi wa meli hizi mbili?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa wananchi wa Mikoa ya Katavi, Kigoma na Rukwa wanategemea meli za MV Liemba na MV Mwongozo: Je, lini Serikali itamaliza ukarabati wa meli hizi ili ziweze kufanya kazi kwenye Ziwa Tanganyika?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpaka tunavyoongea hivi tuko kwenye hatua za mwisho kabisa, na wakandarasi wa kuanza kujenga hizo meli kubwa mbili katika Ziwa Tanganyika walishapatikana. Kwa hiyo, wananchi wawe na imani, na ndiyo maana tunategemea kwamba tunaweza hata tukasaini kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha ili tuanze ujenzi wa hizo meli. Mkataba wa ujenzi, tunategemea watajenga kwa muda wa miaka miwili hizo meli mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali lake la pili, tunatambua kwamba kwa sasa hakuna meli ambayo inafanya kazi katika Ziwa Tanganyika. MV Liemba tunavyoongea imeshapata mkandarasi na mkataba ni kwamba ukarabati huo utachukua miezi minane na meli hiyo itakuwa imerudishwa majini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Meli ya Mwongozo, meli hii ina historia yake. Kilichokuwa kimesimamisha hiyo meli isifanye kazi, siyo kwa sababu ya ubovu, ila Serikali ilitaka ijiridhishe kuhusu stability ya hiyo meli. Tunavyoongea, tayari Serikali ilishamu-engage Mhandisi Mshauri ambaye ni Chuo chetu cha DMI kufanya tathmini, na kama kuna marekebisho, yafanyike. Yakishafanyika, hiyo meli pia itarudi majini muda siyo mrefu. Kwa hiyo, tunategemea katika kipindi cha karibuni meli mbili; MV Liemba na MV Mwongozo zitarudi majini kuanza kufanya kazi katika Ziwa Tanganyika kwa muda wa karibuni sana ahsante. (Makofi)
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Kivuko cha MV Musoma kilitolewa na Serikali na kivuko kilichopo hakikidhi mahitaji na kina changamoto nyingi sana, kinaweza kusababisha matatizo: Je, ni lini Serikali itarejesha Kivuko kile? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa miundombinu ya ujenzi kule Kinesi inahusisha maeneo waliyokuwa wanamiliki wananchi pale Kinesi: Je, lini Serikali itawalipa fidia wananchi wale ili waweze kupisha mradi huo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Mara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Kivuko cha MV Musoma ambacho kilikuwa kinafanya kati ya Mwigobero na Kinesi kilihamishwa kwenda kutoa huduma katika Kivuko cha Kisorya na Rugezi kwa sababu ya ukubwa wake. Kivuko cha Totuu kilitolewa Chato kwenda Musoma kufanya kazi kwa sababu kituo kilichokuwa kinafanya kazi kati ya Nansio kwa maana ya Kisiwa cha Ukerewe na Kisorya kilikuwa kimeharibika na kilikuwa kinahitaji matengenezo makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Mbunge ni kwamba Kivuko cha MV Ujenzi ambacho kinafanya kazi kati ya Rugezi na Kisorya tuko kwenye hatua za mwisho kabisa. Kilichokuwa kinafanyika ni kubadilisha engine, sasa tunapaka rangi. Tunaamini mwishoni mwa mwezi wa Saba, kivuko hicho kitakuwa kimekamilika ili MV Musoma iweze kurudi kwenda kufanya kazi kati ya Mwigobero na Kinesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu matengenezo au ujenzi katika eneo la Kinesi, tayari tumeshafanya tathmini na tumeshaainisha wananchi watakaopisha ujenzi wa maegesho. Hivi tunavyoongea sasa hivi, taratibu za kuandaa majedwali ya kuwalipa zinaendelea ili mwakani tunapoanza tuweze kujenga maegesho upande wa Kinesi pamoja na miundombinu yake, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Wizara ya Ujenzi ilitenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vivuko vipya: Ni lini ujenzi huo wa vivuko vipya utaanza pale Kigamboni?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika mwaka huu unaoendelea, Serikali ilitenga fedha za kujenga vivuko vingi, vikiwemo vya maziwa na vya pale Kigamboni alivyovisema Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa tunategemea kujenga kivuko kimoja kikubwa, lakini pia kumetokea maombi kadhaa na Serikali inafanya tathmini kuona baada ya kupata uzoefu wa vivuko hivi vidogo vya Bakhresa, namna ambavyo tunaweza kufanya ni kujenga kivuko kibwa na pia kuwa na vivuko vidogo. Kwa hiyo, kinachoendelea sasa hivi, tuko kwenye taratibu za manunuzi kuhakikisha kwamba kile tulichokipanga tunakifanya pia katika mwaka huu, pamoja na kuongeza vivuko vidogo ambavyo tumeona vinakwenda kwa haraka sana kati ya Kigamboni na Kivukoni, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara za lami huwa unaboresha sana mazingira na mandhari ya nchi yetu kule inakopita. Barabara hii pale inapoanzia kuna soko la Tengeru ambalo hali yake ni mbaya kimazingira na miundombinu, lakini tunajua kwamba, miradi mikubwa hii ina-component ya CSR.

Je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia Halmashauri ya Meru kuboresha soko hili kwa kutumia CSR yake?

Swali la pili, kwa kuwa, mradi huu uko kwenye hatua ya usanifu na upembuzi yakinifu, Serikali haioni ni busara kuweka uboreshaji wa soko hili katika usanifu huo? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili kwa pamoja ya Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwenye miradi hii mikubwa kunakuwa na component ya CSR. Ninachoweza kumuomba Mheshimiwa Mbunge, tumelipokea ombi lake la kuboresha hiyo miundombinu ya soko la Tengeru pamoja na barabara inayoingia, lakini tu pengine nishauri ni vyema tukapata maombi rasmi ili tuweze kuyaratibu kabla Mhandisi Mshauri hajakamilisha, basi iwe ni sehemu ya mpango wa kuijenga hiyo barabara ikiwa ni pamoja na kujenga hiyo barabara ndogo ya kuingia kwenye soko na kuboresha hilo soko, ahsante. (Makofi)

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini sasa Serikali itajenga barabara ya Singida – Sepuka – Ndago kwa kiwango cha lami ambayo kimsingi ni barabara muhimu sana kwa wananchi na wakazi wa Tarafa ya Sepuka, Jimbo la Singida Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ya Singida – Sepuka – hadi Ndago ni barabara ambayo tunategemea muda wowote kusaini mkataba kwa ajili ya kuanza ujenzi kwani tayari taratibu zote za manunuzi zimeshakamilika. Kwa hiyo, kinachosubiriwa tu ni kuisaini ili ujenzi uanze kujenga barabara hiyo yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.(Makofi)
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, ni lini barabara nne zitajengwa eneo la Nyangole, Bukoba Mjini ili kutimiza ahadi ya Makamu wa Rais?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara nne eneo la Nyangole, ambayo iko Bukoba Mjini ilikuwa ni ombi la Mheshimiwa Mbunge wa Bukoba Mjini, Mheshimiwa Byabato, wakati Makamu wa Rais amefanya ziara katika Mji wa Bukoba. Ninamshukuru kwanza Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge, kwa kuendelea kufuatilia utekelezaji wa ahadi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Oliver pamoja na Mheshimiwa wa Bukoba Mjini na wananchi wa Bukoba Mjini agizo hilo tayari tumeshaanza utekelezaji. Katika hii barabara tutafanya kazi tatu, moja itakuwa ni kuondoa, kupunguza zile kona, kupunguza mteremko, lakini pia kujenga barabara ya njia mbili zinazoshuka na njia mbili zinazopanda, tutaanza na kilometa nne, lakini mpango ni kujenga kilometa tano kutoka hapo Nyangoya hadi Bukoba bandarini. Ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, barabara hiyo ya Kibada hadi Tundwi - Songani inakwenda mpaka Pemba Mnazi ambapo kuna viwanja vingi vimetengwa na Serikali, lakini kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa Barabara. Ukosefu wa kujengwa barabara hiyo unasababisha kuongezeka kwa nauli kwa wananchi wa Kisarawe II, Mwasongwa na Tundwi - Songani.

Je, nataka commitment ya Serikali, ni lini? Je, ni kweli itaanza kujengwa barabara hiyo mwezi Juni, maana imekuwa ni ahadi ya muda mrefu.

Swali la pili, changamoto ya ukosefu wa barabara inaikumba pia Halmashauri ya Ubungo. Barabara ya Victoria – Mbezi – kwa Yusufu hadi Mpiji Magohe. Ni lini barabara hiyo nayo itajengwa?(Makofi)
NAIBU WAZIRI UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na swali la kwanza la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, barabara hii niliyoitaja tunakwenda kuijenga, ndiyo maana bila kusita tunategemea mwezi kabla haujaisha huu wa Juni tuwe tumeisaini kwani Mkandarasi alishapatikana tuanze ujenzi wa barabara hii. Tunatambua umuhimu wa barabara hii kwani sasa limekuwa ni eneo muhimu sana kwa shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa Dar-es-Salaam na hasa Jimbo la Kigamboni. Pia ni kwamba, tunajua alikuwa amepata changamoto ya kuharibika, Mkandarasi tayari yupo site kuanzia Mji Mwema, Kimbiji lakini Mji Mwema - Mwasonga hadi Kimbiji kuhakikisha kwamba, anarudisha barabara kwenye hali yake nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara alizozitaja hizi tayari, kama ataangalia kwenye bajeti za Jimbo la Ubungo, barabara hizi tumeziingiza kwenye mpango. Kulikuwa na barabara moja ilikuwa haijafanyiwa usanifu hasa ile ya Kwa Yusufu - Makabe, lakini barabara nyingine hizi tumeziweka kwenye mpango wa kuanza kuzijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Barabara ya Mbuyu wa Mjerumani – Magara – Mbulu ni muhimu sana inayounganisha Mkoa wa Manyara na Wilaya za Mbulu na Mji wa Arusha: Je, kwa nini Serikali imeshimdwa kutekeleza eneo la mlima Magara ambalo lina jiografia ngumu sana na inatumia gharama kubwa kwa kiwango cha changarawe? Lini itaweka lami mlima Magara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Barabara ya Mbuyu wa Mjerumani – Magara hadi Mbulu ni barabara ambayo inapita kwenye escarpment. Mheshimiwa Mbunge atakuwa ni shahidi kwamba tunachokifanya sasa hivi, ni kukamilisha eneo lote la ule mwinuko kujenga kwa kiwango cha lami au kiwango cha zege. Baada ya kukamilisha hayo maeneo ambayo yamekuwa ni changamoto kubwa, mpango sasa ni kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami, kwani usanifu tayari umeshafanyika, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu la msingi katika swali hili ambalo limetoka kwa Mheshimiwa Mariam Kisangi, umesema kwamba barabara ile inakwenda kujengwa kwa kiwango cha lami, tunashukuru kwa hilo, lakini barabara hii kwa sasa hivi imeharibika sana kutokana na uzito wa magari yanayopita pale pamoja na mvua ambazo zimenyesha: Ni lini ukarabati wa barabara hii utafanyika wakati tunasubiri barabara hii kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Faustine Engelbert Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara nyingi za Dar es Salaam, hasa ambazo ni kwa kiwango cha changarawe, zimepata changamoto kutokana na mvua ambazo zimekuwa zinaendelea kunyesha katika Mkoa wa Dar es Salaam, lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika barabara zake hizo alizozitaja, tayari tumesham-engage Mkandarasi, Ibra Construction Company ambaye amepewa barabara ya kutoka Mji Mwema kwenda Kimbiji na pia huyu huyo atafanya kazi kutoka Kibada – Mwasonga – Kimbiji na kuendelea mbele ili kurejesha mawasiliano na kuondoa changamoto ambazo zinaendelea kwa sasa. Kwa hiyo, mkandarasi tayari ameshakuwa site, ahsante.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Kibiti wamenituma niulize kwa mara nyingine tena, ni nini mpango au mkakati wa Serikali kuhusiana na barabara ya Kibiti – Dimani mpaka Mloka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Twaha Ally Mpembenwe, Mbunge wa Kibiti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii sasa hivi tunairudisha tena kuifanyia review ya usanifu, lakini naamini ndiyo barabara ambayo tayari tunajenga lile Daraja kubwa la Mbambe kuhakikisha kwamba tunaondoa hiyo changamoto. Mpango ni kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, ambayo pia ni barabara fupi sana kwenda Bwawa la Nyerere ukitokea Pwani, ahsante.

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya milimani ya Vudee ni fupi sana, lakini kila mwaka Serikali inamwaga kifusi na mvua inaponyesha, basi inazolewa na maji: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kwamba tukimaliza Bunge twende Vudee milimani ili akaone barabara hii inayokwenda mpaka Ndolwa ili iweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami au zege ili Serikali isipoteze fedha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubalina na Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo ya milimani kwa kweli yana changamoto kubwa. Kwanza nitoe maelekezo kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Kilimanjaro aitembelee hiyo barabara. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya Bunge twende tukaipitie, lakini twende wakati mtaalam ameshapita ili tuwe tayari tuna taarifa za awali kuhusu changamoto ambazo ziko kwenye hiyo barabara. Kwa hiyo nakubali, tutakwenda kuitembelea hiyo barabara, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Watu wa Tarime wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mama wa Taifa, kwa kutoa fedha ya kujenga lami kilometa 25. Sasa naomba nijue: Lini kipande cha kitoka Kwinogo – Nyamongo hadi Serengeti Mugumu kitaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, tulishaongea na Mheshimiwa Mbunge, na kweli kipande hicho tutakijenga kwa kiwango cha lami. Tayari mkandarasi alishapatikana, taratibu za manunuzi zimeshapatikana. Tunachofanya sasa katika maandalizi ni kutafuta siku ya kusaini kipande kilichobaki cha kutoka Nyamwaga hadi Mugumu - Serengeti kwa kiwango cha lami.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali hili hili ambalo limeulizwa na Mheshimiwa Mbunge wa Tarime Vijijini, nimeuliza mara nyingi na ni mara nyingi nimeongea na Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu barabara hii ya Nyamongo mpaka Mugumu: Sasa tunaomba kujua ni lini hasa kwa maana ya tarehe, utakaposainiwa huo mkataba na kuanza ujenzi wa barabara ya Nyamongo – Mugumu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu niwafahamishe Waheshimiwa Wabunge, na hasa Mbunge wa Tarime na Mbunge wa Serengeti, hii barabara inaunganisha Serengeti na Tarime, lakini kutoka Serengeti pia inategemea kwenda Nata. Naomba wawe na Subira. Taratibu zote za manunuzi zimeshakamilika, tunachosubiri ni kutafuta siku maalum ya kufanya signing.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuna hakika, kama utaratibu utakwenda kama tulivyopanga ni kuisaini hiyo barabara kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha. Kwa hiyo, siku itakapokuwa tayari, tutawajulisha Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mbunge wa Serengeti na Mheshimiwa Mbunge wa Tarime Vijijini, ahsante.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukifika Chalinze kuna roundabout nzuri kuliko roundabout yoyote hapa nchini, lakini pale kuna kilometa 25 kufika Magindu: Ni lini barabara ile itajengwa kwa kiwnago cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tushukuru kwamba keep left ile ni kati ya keep left nzuri katika nchi yetu. Hiyo barabara aliyoitaja ya Chalinze – Magindu katika bajeti inayokuja imepangwa ifanyiwe usanifu yakiwa ni maandalizi ya kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Sisi tuna barabara ya kutoka Namtumbo – Mtonya – Mgombasi, kuna daraja katika Mto Luwegu ambalo linahatarisha maisha ya watu, kwani ni jembamba sana: Je, Serikali inaweza kuiwekea fedha kulijenga daraja hilo ili kuepusha maafa yanayoweza kutokea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwanza nipokee ombi la Mheshimiwa Mbunge kwa sababu daraja hilo linahatarisha maisha ya wananchi. Pia nimwelekeze Meneja wa TANROADS Mkoa wa Ruvuma ili aiangalie hiyo barabara kwa maana ya Namtumbo – Mto Luwegu hadi Mgombasi, pia akaangalie daraja hilo, afanye tathmini, halafu alete Makao Makuu kwa ajili ya kutafuta fedha kulijenga hilo daraja la Mto Luwegu, ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa Serikali imejenga madaraja mazuri kwenye barabara ya Lupila kwenda Ikonda: Je, lini mtajenga kwa kiwango cha lami ili kukamilisha kazi ile nzuri na wananchi wetu wakaweza kupita vizuri kwenye barabara ile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, azma ya Serikali ni kujenga hizi barabara kwa kiwango cha lami. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwa kuwa tumeshaanza kujenga hii barabara nzuri, tutahakikisha tunaifikisha mwisho ikiwa ni pamoja na barabara aliyoitaja kuijenga kwa kiwango cha lami kulingana na upatikanaji wa fedha, ahsante.

MHE. PROF KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Barabara ya Kimara – Mavurunza mpaka Segerea imewekwa kwenye bajeti ya mwaka huu, lakini kwa sasa haipitiki, hali yake ni mbaya sana: Kwa nini Serikali isifanye matengenezo wakati tukisubiri ujenzi wa lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Prof. Kitila Alexander Mkumbo, Mbunge wa Ubungo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema, barabara za Dar es Salaam nyingi ambazo siyo kwa kiwango cha lami ziko kwenye mazingira magumu. Nimwagize Meneja wa TANROADS Mkoa wa Dar es Salaam, aende kwenye barabara hii ambayo inaunganisha Jimbo la Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo na Mheshmiwa Bonnah, waende wakaiangalie ili waweze kuondoa hizo changamoto na waweze kurejesha usafiri kati ya hayo majimbo mawili, ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi. Serikali ya Awamu ya Tano iliahidi kuwajengea wananchi wa Minziro barabara ya kutoka Mutukula kwenda mpaka Minziro, na ni faraja kwamba Naibu Waziri alikuja akatembelea barabara hiyo na sasa hivi imeanza kufumuliwa: Je, lini sasa barabara hiyo itakamilika kwa kiwango cha lami kutoka Mutukula kwenda Minziro?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, barabara hii tulitembea na Mheshimiwa Mbunge, mimi nilishaitembelea. Kitu cha kwanza kilikuwa ni kuifungua hiyo barabara, na kitu cha pili tutakachofanya sasa ni kuifanyia usanifu. Ni barabara muhimu kwa sababu ipo kwenye uchumi na pia ni barabara ya ulinzi ambayo ni moja ya vipaumbele vya kujenga barabara kwa kiwango cha lami kwa mujibu wa sera zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya kuifungua yote tutaifanyia usanifu ikiwa ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini kwa uhalisia hawa Maafisa Ustawi wanakua hawapo kwenye hivi vivuko wakati watu hawa wanatumia huduma hii. Nini kauli ya Serikali kwa vivuko vyote nchini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala hili halijatamkwa wazi kwenye Sheria ya Leseni za Usafirishaji Nchini. Nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba suala hili linatamkwa wazi kwenye Sheria hii ya Leseni za Usafirishaji Nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, ni kweli kwamba hatuwaweki watu wa ustawi wa jamii kwenye vivuko lakini tunachotaka wafanye ni kwamba waende kwenye ofisi za Wakuu wa Wilaya pamoja na ofisi za ustawi wa jamii ambapo wanapewa barua ama vibali kwamba waweze kusaidiwa kwa sababu hawana uwezo hivyo waweze kuvuka kwenye vivuko ama kutumia kwenye vivuko kwa kupunguziwa ama bila kulipa, ndiyo maana tumesema Waheshimiwa Wabunge waendelee pamoja na Wakuu wa Wilaya na watu wa ustawi kuwafahamisha watu wenye ulemavu ama mahitaji maalum kwenda kabla hajaanza safari basi apate kile kibali ama barua ambayo atakapofika kwenye kivuko husika hatabughudhiwa na hilo limekuwa likifanyika.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la kutamka kisheria, kulipa ama kutolipa kwa watu wenye ulemavu linategemea na uwezo. Watu Wenye Ulemavu, kuna ulemavu wa aina mbalimbali, wako wenye ulemavu ambao kimsingi wana uwezo nadhani hapa tunachoongela kupunguza ama kutolipa ni wale kabisa ambao wamethibitika hawana uwezo na ndiyo maana pengine wanatakiwa waende kwenye ofisi husika ambao watasema kweli huyu hana uwezo kwa hiyo hastahili kulipa, lakini wale wenye uwezo nadhana ndiyo maana sheria haikutungwa ili waweze kulipa.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo kama kutakuwa na umuhimu nadhani tunazo sekta mbalimbali ambazo zinashughulikia hawa Watu Wenye Ulemavu labda sasa litachukuliwa na Serikali liangaliwe kama kuna haja ya kulitungia sheria. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa kuwa watu wenye ulemavu kwanza kwa idadi siyo wengi, lakini wengi wao hupata changamoto hata ya kuwa na kipato: Ni kwa nini kusiwepo na tamko dhahiri kwamba kila mwenye ulemavu at least unaoonekana aweze kuvuka bure kwenye vivuko ili kuwapunguzia adha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, nimesema watu wenye ulemavu wanatofautiana kwa kiasi kikubwa sana, na wapo watu wenye ulemavu ambao wana uwezo pengine kukuzidi hata wewe Mheshimiwa Mbunge. Sasa ukisema tu mtu mwenye ulemavu yeyote asilipe, nadhani pia tutakuwa hatuwatendei haki. Tumesema watu wenye ulemavu ambao kweli vyombo vinaweza vikatambua huyu hana uwezo kwa kweli, hao wanatakiwa wasaidiwe, ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza naishukuru Serikali, imesikia kilio cha wananchi wa Mbozi na Momba kwa kutenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi huo.

Swali langu la kwanza; je, ni kilomita ngapi sasa Serikali itaanza kwa awamu hii?

Mheshimiwa Spika, pili; je, ni lini mchakato wa kumpata mkandarasi utaanza ili ujenzi uanze? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hiyo yenye urefu wa kilometa 147 kwa mwaka ujao wa fedha tumepanga kuanza kuijenga kilometa 50.

Swali lake la pili kuhusu ni lini tutaanza, barabara hii tutaanza kuijenga ama kutafuta mkandarasi tutakapoanza utekelezaji wa bajeti wa 2023/2024, na ndipo tutakapoanza kutekeleza mpango huu wa kuanza kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa fursa hiyo. Kwanza tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kukubali kuanza kusaini kesho barabara karibu nane kwa mfumo wa EPC and F, maana Bungeni hapa imezungumzwa muda mrefu kuhusu hilo suala; je, mara baada ya kutangaza habari ya kusaini hiyo kesho, ni lini ujenzi utaanza kwa barabara hizo ikiwemo Mafinga – Mgololo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza niseme, barabara ambazo tunategemea kutia sahihi ni barabara saba. Pengine tu nilijulishe Bunge hili kwamba kazi kubwa ambayo tulikuwa Mheshimiwa Rais anakwenda kuifanya ni kusaini mikataba ya hizi barabara zote saba ambazo tumeziongelea sana hapa za EPC + F na kazi hiyo itafanyika kesho hapa Dodoma Jakaya Kikwete. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu pengine Wabunge wengine hawajapata taarifa, tungetamani pia Wabunge wote ambao hizo barabara zinapita waweze kushuhudia kitu kikubwa ambacho kinafanyika kuanza kujenga hizo kilometa 2,035 kwa mpigo. Muda ungetosha ningeweza kuwakumbusha zile barabara lakini kwa sababu ya muda, ni hizo barabara zote saba ambazo kwa ruhusa yako labda niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge ni barabara ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Ifakara – Lupilo – Malinyi – Kilosa – Kwa Mpepo hadi Lumecha Namtumbo, nyingine ni barabara ya Igawa – Mbeya Mjini – Songwe hadi Tunduma, barabara ya Kongwa – Kibaya – Orkesumet – Rosinyai hadi Arusha, barabara ya kutoka Karatu - Mbulu – Hydom – Sibiti – Lalago hadi Maswa na mwisho ni barabara ya Mafinga – Mtwango – Mgololo, ahsante. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali iko tayari kutenga fedha katika mwaka wa fedha wa 2024/2025 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Ni lini Serikali itasaini mkataba na wakandarasi kwa ajili ya ujenzi wa kilomita nane za barabara ya lami ya Dareda Center kwenda Dareda Mission ikiwa sehemu ya kwanza ya ujenzi wa barabara hiyo kutoka Dareda kwenda Dongobesh? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ndiyo inayounganisha Makao Makuu ya Mji wa Manyara, Babati na Wilaya mbili ya Kiteto na Simanjiro. Kwa hiyo, ni wazi kama tulivyosema kwenye mpango wetu kwamba tutaziunganisha hizo barabara kwa kiwango cha lami, kwa hiyo, naamini kwa mwaka wa fedha utakaokuja, hizi barabara zitaingia kwenye mpango na ndiyo maana sasa hivi tunakamilisha usanifu wa kina.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Dareda – Dongobesh ambayo tutaijenga kwa kuanza na kilomita nane, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu za manunuzi zimekamilika na tunategemea pengine kabla ya tarehe 22 kama taratibu zitakwenda kama tulivyopanga, mkandarasi awe ameonyeshwa site kuanza ujenzi wa hizo kilomita nane, ahsante. (Makofi)
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imefanya mapinduzi makubwa ya kutumia utaratibu wa EPC + Financing na kesho inasainisha mikataba saba hiyo; je, ipo tayari kuifikiria barabara ya Makofia – Mlandizi – Mzenga – Mwanarumango kwenye utaratibu huo siku za usoni? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ni wazi kwamba hii barabara aliyoitaja tumekuwa tunaitengea bajeti na bado hatujakamilisha kulipa fidia hasa kwa kipande cha Makofia hadi Mlandizi, lakini mpango ni kuijenga hii barabara yote kwa kiwango cha lami. Sasa kama itaingia kwenye utaratibu wa kawaida ama utaratibu wa EPC + F itategemea na kipindi hicho ambapo sasa tutaanza kuijenga hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, wakati najibu barabara za EPC nilisahau pia kuwakumbusha watu wa kuanzia Handeni – Kiberashi – Kibaya – Kwamtoro hadi Singida, pia hiyo barabara itakuwepo kesho, ahsante. (Makofi)

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Daniel Awack nashukuru sana Serikali kwa majibu yake mazuri, lakini nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, je, ni lini barabara ya kutoka Redio Habari Maalum kwenda Hospitali ya Wilaya ya Arumeru itajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, moja ya maeneo ambayo tunayafanyia kazi sana ni pamoja na kupeleka barabara za lami kwenye maeneo yanayotoa huduma za jamii kama hospitali.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ya Ujenzi pamoja na wenzetu wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa tutashirikiana kuhakikisha kwamba hii barabara ambayo ni fupi sana kilometa tatu inafanyiwa usanifu na kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa na mimi swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Magugu – Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu ni barabara muhimu sana kwa wakazi wa Mbulu na Babati, lakini kipande cha Mbuyu wa Mjerumani – Mbulu ni hatarishi sana kwa kipindi cha mvua.

Sasa ni lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mbuyu wa Mjerumani – Daraja la Magala hadi Mbulu imeshakamilishwa kufanyiwa usanifu wa kina na tayari daraja tumeshajenga. Tunachofanya sasa hivi kwenye hii barabara ni kujenga kwa kiwango cha zege maeneo yote hatarishi na hasa kwenye escapement, lakini wakati huo tukiwa tunatafuta fedha kujenga barabara yote hii kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, barabara kutoka Mombo – Soni – Lushoto ni barabara nyembamba sana, ni mlimani, ni kona kali na imewekewa mpango kwa ajili ya kupanuliwa. Nataka kujua, je, mpango huo bado upo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nakiri na mimi nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara aliyotaja ya Mombo hadi Soni ni barabara ya lami ilijengwa zamani na ni nyembamba sana na ipo kwenye miinuko. Ni kweli kwamba Serikali ina mpango wa kuiboresha kwa maana ya kuipanua, kupunguza kona na kupunguza ile miinuko ili barabara hii iwe salama kwa watumiaji wote wanaoitumia kutoka Mombo kwenda Lushoto na Mlalo, ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, Bagamoyo, Kibaha Mjini na Kisarawe wamepewa ahadi ya ujenzi wa barabara yao ya lami ya Makofia – Mlandizi – Kisarawe kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi hii inayoendelea.

Je, ni lini itaingia kwenye kusainiwa mikataba kama ilivyofanywa barabara za juzi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu sana kwa maendeleo yetu na hasa inayounganisha barabara ya Bagamoyo na hii barabara ya Morogoro. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kitu cha kwanza ambacho kitafanyika kwanza ni kulipa fidia kwa wananchi ambao tayari walishaainishwa ili waweze kupisha barabara na tumetenga fedha kwa mwaka ujao kwa ajili ya kuanza hiyo barabara ya Makofia – Mlandizi kwenda Mzenga huko Kisarawe, ahsante. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kutokana na umuhimu wa barabara hiyo katika kuchochea uchumi wa wananchi wa Urambo, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami ikitokea Kahama – Ulyankulu – Urambo – Ussoke – Tutuo – Sikonge ili waendelee wasafiri mpaka Mbeya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kadri tunavyofungua nchi na kuunganisha miji barabara aliyoitaja ni muhimu sana hasa kwa sababu itapunguza sana urefu wanaosafiri watu wa kutoka Kahama na hata watu wanaotoka njia ya Kigoma ambao kama wanaenda Mbeya hawana sababu ya kupita Mjini Tabora. Ndio maana tumesema tunaendelea kuhakikisha kwamba tunafanyia usanifu hiyo barabara ya kutoka Ulyankulu hadi Urambo na kipande cha Ussoke hadi Tutuo ili kuwapunguzia wananchi hawa umbali mrefu wa kusafiri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kinachotakiwa sasahivi tunatafuta fedha sasa ili barabara hii ifanyiwe usanifu na ijengwe kwa kiwango cha lami kwa ajili ya kufungua hilo eneo la Wilaya ya Urambo, lakini pia na kuunganisha na Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara ya kutoka Mbamba Bay hadi Lituhi imo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kujengwa kwa kiwango cha lami. Je, Serikali imefikia wapi katika suala hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, barabara aliyoitaja ina sifa mbili, kwanza ni barabara ya ulinzi lakini pia ni barabara ambayo inaambaa ambaa na ziwa kutoka Mbamba Bay kwenda Lituhi. Barabara hii tulishafanya usanifu na sasa kinachotafutwa ni fedha ili kuijenga kwa kiwango cha lami ambapo itaunganisha Bandari ya Mbamba Bay ambayo tayari kuna lami, lakini na Lituhi ambako sasa Mheshimiwa Mbunge anakubali tunajenga kuanzia Amani Makolo mpaka Bandari ya Ndumbi. Kwa hiyo, kipande kilichobaki hapo tukishaunganisha tutakuwa tumekamilisha barabara za lami na itakuwa ni rahisi sana kufanya ulinzi, lakini pia kufungua Wilaya ya Nyasa, ahsante.

MHE. ALLY A. J. MLAGHILA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishukuru sana Serikali ya Chama cha Mapinduzii kupitia Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa ujenzi wa barabara hii na kwamba sasa imeanza. Sasa, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; je, Serikali imejiridhisha na uwezo wa Mkandarasi huyu mpaka kumpata maana inachoonekana sasa ni kwamba mkandarasi anasuasua sana tangu alipopewa ile site?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi wote ambao wamepitiwa na barabara hiyo tangu miaka mitano iliyopita waliambiwa wasiendeleze maeneo yao na mpaka sasa hivi hawajalipwa maeneo yao na bado hawajapewa hata kiasi chochote au karatasi lolote linaloonesha kwamba wanaweza kulipwa kiasi fulani. Je, ni lini Serikali itawalipa wananchi wanaopitiwa na barabara hii pesa zao za fidia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Anyigulile Jumbe Mlaghila, Mbunge wa Kyela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kyela kwamba Mkandarasi ambaye amepewa kazi hii ana uwezo wa kutosha ndiyo maana amepewa kazi hiyo. Vile vile, ni mkandarasi ambaye alifanyiwa due diligence kwa maana ya kuangalia uwezo wake wa kifedha kwa maana ya mtaji lakini pia na vifaa vya kufanyia kazi hiyo. Kwa hiyo, tunaamini uwezo huo anao na ataijenga hiyo Barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili la fidia. Ni kweli wananchi hawa bado hawajalipwa fidia, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kyela kwamba uthamini ulishakamilika na majedwali ya malipo yalishakamilishwa na tayari Wizara ilishapeleka uthamini kwa maana ya gharama watakazolipwa ambayo ni bilioni 1.734 kwa wananchi wanaostahili kulipwa, hususani wale ambao watapisha ujenzi huu na watalipwa kwa mujibu wa Sheria yetu ambayo tunaituma kwa watu wanaopisha ujenzi wa barabara, ahsante.
MHE. KABULA E. SHITOBELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, je, ni lini ujenzi wa Barabara ya Hungumalwa – Kwimba kwenda Magu utaanza?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shitobela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara aliyoitaja ya Hungumalwa – Ngudu – Bukwimba hadi Magu ni barabara ambayo kumekuwa na watu wengi ambao wameipigia kelele sana. Hata hivyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, katika mwaka wa fedha ambao bajeti tayari imeshapitishwa barabara hii imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kwa sababu usanifu ulishakamilika tayari, ahsante.

MHE MASHIMBA M. NDAKI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Njia Panda - Ikungu kwenda Malampaka kilometa 14 au 15 inajengwa kwa lami, leo ni mwaka wa sita lakini zimejengwa kilometa nne tu. Sasa naomba kujua ni lini Serikali itatenga kiasi cha pesa cha kutosha ili kuweza kukamilisha ujenzi wa barabara hiyo ambayo ni muhimu kuunganisha Mkoa wa Simiyu na Kituo kikubwa cha SGR pale Malampaka?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kuhusu swali lake la muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja ni kweli ndio barabara ambayo inaunganisha SGR, Mkoa wa Simiyu na hata watu ambao wanaweza kwenda na ndio kituo sahihi na hiyo barabara ndiyo inayounga. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali itafanya kila kinachowezekana kuhakikisha kwamba ahadi iliyoitoa ya kujenga hizo kilometa 14 ambazo bado kilometa 10 tunaikamilisha ili kuhakikisha kwamba Kituo cha Malampaka kitakuwa ni muhimu sana kwa wananchi wa Maswa na Bariadi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inafahamu na itahakikisha kwamba inaijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Hivi sasa kampuni ya Kichina inatekeleza ujenzi wa barabara ya lami kutoka Mbulu kwenda Garbabi kilometa 25, lakini barabara hiyo kwa jiografia ya milima inahama kwenda nje ya mita 22.5 kutoka katikati ya Barabara: Je, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka wa kwenda kuwaelimisha wananchi ili tujue wanaofidiwa na wasiofidiwa ndani ya corridor hiyo ya barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia Paul Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ulivyo utaratibu kwamba pale ambapo tunajenga barabara tunatumia sheria za barabara na hasa kwenye kutoa fidia. Kwa wananchi ambao wako ndani ya mita 22.5 kutoka katikati ya barabara kwa pande zote wanakuwa wako kwenye hifadhi, lakini wale ambao wako mita 7.5 kwa pande zote ambazo zimeongezeka, barabara inakuwa imewafuata, na hao kwa kweli wanatakiwa wafanyiwe tathmini, waainishwe na walipwe fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nina hakika kama hivyo ndivyo, Mheshimiwa Mbunge suala hilo litafanyika kwa hao wananchi wa Mbulu hadi Garbabi, ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba kufahamu kwenye mikataba iliyosainiwa, barabara ya Hydom – Mogitu yenye urefu wa kilometa 68, ipo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Haydom – Mogitu ilikuwa ni sehemu ya barabara ya Serengeti Southern Road wakati wa design ya awali, lakini katika mpango huu wa EPC + F barabara hii kwa sasa tunaifanyia usanifu, maana ilikuwa imefanyiwa usanifu wa awali, sasa tumeiingiza tuifanyie usanifu ili tutakapokamilisha hiyo barabara ambayo ni ya EPC + F tuweze kuijenga hiyo pia kwa sababu ndiyo inayounganisha barabara ya Hydom kwenda Sibiti na barabara ya Singida kwenda Babati, ahsante.

MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Dumila kwenda Kilosa, kutoka Kilosa kwenda Mikumi kupitia Masanze – Zombo – Ulaya na Muhenda mpaka Mikumi ni uti wa mgongo kwa uchumi wa Mkoa wa Morogoro: Nini Kauli ya Serikali kuhusiana na hali ya barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakubaliana na Mheshimiwa Londo kwamba, kwa kweli hiyo ni barabara muhimu sana na hasa tutakapokamilisha hii barabara ya kutoka Lumecha – Malinyi – Kidatu hadi Mikumi. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba, kwa sababu ya umuhimu wake, katika bajeti inayokuja tumeitengea fedha ili kuendelea kuijenga kwa kiwango cha lami ili kuunganisha Kilosa na Mikumi kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini barabara ya Chombe – Kaoze – Igonda mpaka Ilemba itajengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, Rukwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu cha kwanza ni kuifanyia usanifu wa kina hiyo barabara halafu baada ya hapo Serikali itajua gharama halisi ya kuijenga hiyo barabara na ndiyo sasa tutaiingiza kwenye mpango wa kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniona. Barabara ya Igawa – Kinyanambo – Mafinga huko imefanyiwa upembuzi yakinifu kwa muda mrefu na iko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi pia: Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Igawa – Kinyanambo ipo kwenye ilani na kwa kweli, inatakiwa ijengwe kwa kiwango cha lami hasa tukizingatia umuhimu wa barabara hii inayopita maeneo yanayozalisha sana hasa mpunga. Serikali inaendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa mpango uliopo ni kuhakikisha kwamba inafanyiwa ukarabati iweze kupitika kwa kipindi chote cha mwaka. Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba Serikali imeendelea kujitahidi sana kuhakikisha barabara hii inafanyiwa matengenezo mara kwa mara na kupitika kwa muda wote wa mwaka, ahsante.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Je, ni lini barabara ya Oldiani – Mang’ola – Matala – Lalago itajengwa kwa kiwango cha lami na kuwa ni barabara inayounganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu? Ni Sera ya Wizara ya Ujenzi kuunganisha Mkoa kwa Mkoa. Ni lini ujenzi wake utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Awack, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyotaja ni kweli, ni barabara kuu, lakini mpango wa Serikali kwa sasa ni kutafuta fedha kwanza kuijenga kutoka Oldiani mpaka Mang’ola kwenye eneo ambalo wanazalisha sana zao la vitunguu. Kadri tutakavyopata fedha, basi tutaendelea kutoka Mang’ola hadi Sibiti kwa kiwango cha lami, lakini kwa sasa Serikali tunafikiria kuijenga kwa kiwango cha lami Oldiani Junction mpaka Mang’ola, ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Barabara ya kutoka Ipogolo kwenda Kilolo imekuwa ikiendelea kutafutiwa mkandarasi kwa muda mrefu. Napenda kujua ni hatua gani zimefikiwa na ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza? Hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Barabara ya kutoka Ilula hadi Kilolo ambayo kipindi cha mvua huwa inakuwa imeharibika na Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye majibu yake aliahidi kwamba itafanyiwa matengenezo, hadi sasa kuna maeneo bado: je, ni lini matengenezo hayo yatafanywa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Ipogolo – Kilolo yenye urefu usiopungua kilometa 33 ipo kwenye mpango wa kujengwa kwa kiwango cha lami kwa Mradi wa Rise. Tunapoongea sasa hivi Mbunge atakuwa na wananchi wa Kilolo wanafahamu kwamba, iko kwenye hatua ya manunuzi kwa ajili ya kuanza kujengwa barabara yote kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya pili aliyoitaja ya Ilula – Kilolo ambayo anasema mara nyingi inaharibika, ni kweli, eneo hili lina mvua nyingi, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, baada ya kipindi hiki cha mvua kwisha wakandarasi wapo, watakuwa muda wote wanaingia site kwa ajili ya kuikarabati hii barabara kwa kiwango ambacho itapitika bila matatizo, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara inayotoka Tabora Mjini kupitia Mwanza Road ambayo inapita Bwawa la Igome mpaka kwenda Mambari - Nzega, ni muda mrefu haina lami na imekuwa ikisuasua: Lini Serikali itajenga barabara hiyo kwa lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli alichosema Mheshimiwa Mbunge wa Tabora. Nataka tu nimjulishe Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye ilani na tumeitengea fedha kwa ajili ya kuanza maandalizi ya kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, majibu yanaonesha kwamba usanifu utakamilika mwezi Machi, 2024. Sasa kwa kuzingatia umuhimu wa hii barabara ina hospitali kubwa ya Mabwepande ambayo kama wagonjwa wakizidiwa pale wanapelekwa referral Hospitali ya Mloganzila.

Sasa nataka commitment ya Serikali kwamba kwa mwaka ujao wa fedha 2024/2025 kwa sababu usanifu utakuwa umekamilika je, fedha zitaanza kutengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii? Hilo swali la kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, kuna barabara ya Old Bagamayo ambayo inaanzia Morocco, Mwai Kibaki, Daraja la Mlalakuwa pale, Kawe Round About mpaka Afrikana; hii imekuwa ni ahadi ya muda mrefu sana ya upanuzi wa ile barabara, na kuna foleni kubwa sana pale, nataka vilevile kupata commitment ya Serikali kuwa ni lini upanuzi wa ile barabara utafanyika ili kupunguza kero ya foleni kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba hii barabara ya Bunju B – Mabwepande hadi Kibamba ni barabara muhimu sana na imekuwa ikiulizwa mara kwa mara hapa Bungeni na Waheshimiwa Wabunge ambao barabara hiyo inapita kwao akiwemo Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo ambapo wiki iliyopita niliulizwa swali hili.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sio tu tunafanya usanifu wa kujenga barabara kama ya barabara ya kawaida kama alivyosema tunajua kuna hospitali, lakini pia tunajua barabara hii kwa sababu pia kuna Kituo cha Mabasi cha Magufuli kitatumika kwa umakini mkubwa sana itakapojengwa barabara hii.

Mheshimiwa Spika, barabara hii nataka nimjulishe Mheshimiwa Mbunge si tu kwamba itaishia hapo lakini ita–save kama barabara ya mzunguko wa nje kwa Dar es Salaam ambayo itatoka hapo Kinamba – Pugu – Toangoma hadi Kigamboni ndio maana huu muda umekuwa mrefu. Kwa hiyo, hako kaeneo alikouliza ni sehemu tu ya hiyo barabara.

Kwa hiyo, commitment ya Serikali ni kuhakikisha kwamba barabara hii tunaijenga kwa sababu sasa tunajua umuhimu wake ni mkubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kuhusu hizi barabara alizosema za kufanya upanuzi kwa sababu ya misongamano, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara alizozitaja tumeziainisha vizuri sana katika kitabu chetu cha bajeti barabara zote za kupunguza misongamano ikiwa ni pamoja na kupanua. Katika kitabu chetu cha bajeti cha mwaka huu barabara nyingi za Dar es Salaam tutazipanua ambazo zinapatikana katika ukurasa wa 259 – 261 atazikuta hizi barabara zote na nini tunafanya katika mwaka huu huu wa fedha ambao tunauendea wa 2023/2024, ahsante sana.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniruhusu niulize swali moja la nyongeza.

Ni lini Serikali itajenga barabara ya mwendokasi yaani BRT - 4 ambayo kipande kikubwa kinaanzia Mwenge - Makongo Sekondari, Lugalo Jeshini, Mbezi Beach, Tegeta kwa Ndevu, Nyaishozi mpaka Basihaya ambayo pia itaondoa mafuriko yanayoikumba Basihaya kwa kujenga mitaro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gwajima, Mbunge wa Kawe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nataka nimjulishe Mheshimiwa Mbunge wa Kawe kwamba barabara aliyoitaja iko kwenye BRT - 4 ambayo itaanzia Maktaba itakuja Mwenge mpaka pale Daraja la Kijazi hiyo itakuwa ni Lot ya kwanza; na Lot ya pili itaanzia Mwenge – Tegeta mpaka kuja huku DAWASA.

Kwa hiyo, tutakuwa na wakandarasi wawili; lot ya kwanza ndiyo hiyo na lot ya tatu itakuwa ni mkandarasi ambaye atajenga majengo.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tarehe 30 Juni, 2023 siku ya Ijumaa pale DAWASA tunakwenda kusaini mikataba hiyo ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo ya BRT - 4, ahsante sana. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa fedha ambazo zilikwenda kukamilisha ujenzi ule na usimamizi wa Engineer Masige pamoja na Mkuu wa Mkoa barabara ile hatimaye ikakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru pia kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ni lini itaanza ujenzi wa barabara kutoka Katumba – Kapugi - Ushirika? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara kutoka Kiwira – Isangati kutokea Mbalizi ambao huo ni mpango ulio kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suma Ikenda Fyandomo, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nikianza na barabara ya kwanza bahati nzuri hizi barabara zote nazifahamu mimi binafsi, lakini Barabara ya kwanza ya Katumba – Kapugi hadi Ushirika hii barabara bado ilikuwa haijafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina na Meneja wa Mkoa hii ni pamoja na Kiwira na Isangati ameshaanza kuzitembelea hizo barabara ili aweze kubaini gharama za kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa barabara yote ya Katumba – Kapugi - Ushirika lakini pia Ushirika – Isangati - Mbalizi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hapo sasa ndiyo Serikali itaanza kufikiria kuijenga kwa kiwango cha lami baada ya kukamilisha usanifu wa kina, ahsante. (Makofi)
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi; je, ni lini barabara ya kutoka Kimo – Iponjola – Ikuti – Ibungu mpaka Kafwafwa itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantona, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hiyo ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa wa Mbeya kwa maana ya Wilaya ya Rungwe na Wilaya ya Ileje na katika mwaka huu wa fedha tunaouendea imetengewa Bajeti kwa ajili ya kuanza kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kutoka Ibungu – Katengele – Kafwafwa hadi Kimo, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Mji wa Njombe kwa sababu ya wingi wa malori unahitaji kuwa na bypass. Je, ni lini Serikali itaanza kufanya bypass kutoka Kibena kwenda mpaka Yakobi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tulishatoa maelezo hapa kwamba tuna mambo mawili tutafanya. Moja, kuanzia hapo Kibena tunategemea kujenga barabara za njia nne kwa ajili ya kupunguza msongamano, lakini pia sasa hivi Meneja wa Mkoa kulingana na ukuaji wa Mji wa Njombe wameanza kufanya study ya kuona wapi barabara ya bypass itapita na hasa tukizingatia kwamba Mji wa Njombe umekua, kwa hiyo wanaangalia maeneo ambayo hawataingia gharama kubwa ya kutoa fidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo sasa hivi wako wanatembea, baada ya hapo sasa wataweka hiyo ramani kwenye maandishi kwa ajili ya kuiombea fedha kuanza hiyo kazi ya kutengeneza hiyo bypass, ahsante. (Makofi)
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, Barabara ya kutoka Iyombwe – Kisanga – Malolo mpaka Kilolo ni barabara ambayo inahudumiwa na TAZAMA lakini ni barabara muhimu sana ya kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Iringa.

Je, Serikali ina kauli gani kutumia barabara hii kama mbadala wa barabara kuu ya kutoka Mikumi kwenda Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyotaja ni kweli ni muhimu na kwa sasa Serikali inachofanya ni kuhakikisha kwamba inakarabatiwa kwa kiwango cha changarawe wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuifanyia usanifu ikiwa ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY. A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, mwaka 2018 Mheshimiwa Rais aliahidi kujenga Barabara ya kutoka Mbambo – Ntaba – Ipinda; je, Serikali imefikia wapi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Mlaghila, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema kwamba Kiongozi wa Taifa alishaahidi, atakubaliana nami kwamba barabara hii tayari imeshafanyiwa usanifu wa kina na sasa Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)

MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na ningependa kuwa na maswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kutambua umuhimu wa ulinzi na usalama wa mpaka ule wa Ziwa Nyasa na vivutio vya utalii, nini mkakati wa Serikali kuongeza fedha ili kasi ya ufunguaji wa barabara hii iongozeke?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nini mpango wa Serikali kuongeza fedha kwenye barabara inayoanzia Mlangali – Lupila – Makete ili vikwazo vya eneo la Lusala na Ng’elamo viweze kuondolewa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba umuhimu wa barabara hii ukiachilia mbali kwamba ni barabara ya ulinzi, lakini pia wananchi wanaoishi kando kando ya ziwa hawana namna nyingine ya kuwasiliana panapokuwa kuna changamoto ya usafiri wa majini, ndiyo maana Serikali imeanza kwa awamu. Hata hivyo, mpango wa Serikali ni kutafuta fedha ambayo itaifungua hii barabara yote ambayo nimeielezea kwamba ni barabara ambayo inapita kwenye milima na mabonde makubwa sana. Kwa hiyo mpango huo upo ndiyo maana tumeanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu hii Barabara ya Mlangali kwenda Ikonda najua ni muhimu sana kuunganisha Ludewa na Makete na hasa Hospitali ya Ikonda. Serikali imetenga fedha mwaka huu kuhakikisha kwamba maeneo yote yale korofi inakarabatiwa ili iweze kupitika kwa kipindi chote, ahsante. (Makofi)
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Kampuni hii ya Henan Highway Engineering Group iliyopewa kipande cha Handeni – Mafuleta kilometa 20, umepita mwaka mzima sasa tangu kampuni hii ipewe kandarasi hiyo, lakini ujenzi unasuasua. Kwa nini ujenzi huu unasuasua na unaenda kwa kuchelewa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza; ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Turiani – Mziha – Handeni kilometa 104 kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli mkandarasi hajaenda kwa speed ama kwa kasi ambayo tulikuwa tunaitegemea na hii ni kutokana na sababu kadhaa. Moja ya sababu wakati amekabidhiwa barabara hii kulikuwa na changamoto kubwa sana ya mahali pa kutolea materials ambayo ilichukua muda mrefu sana mpaka ku-acquire hilo eneo kwa sababu lilikuwa na mgogoro. Kwa sasa suala hilo limeshakamilishwa na sasa anaendelea kupata yale material ambayo alikuwa anahitaji kutoka kwenye hiyo sehemu ya kutolea materials.

Mheshimiwa Spika, suala lingine kulikuwa na changamoto kwenye management ya kwake, lakini hilo suala pia limeshakamilishwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama alivyomsikia Waziri wa Fedha madai yale ya wakandarasi akiwepo huyu mkandarasi wa barabara hii ya Handeni – Mafuleta malipo yao yatatolewa ili waweze kuendelea, lakini pia wanapokuwa wanapewa kazi hawa wakandarasi moja ya sifa ni uwezo wao kifedha na hatutegemei akiwa 11% aweze kusimama, anatakiwa aendelee lakini pia vifaa ikiwa ni pamoja na management yake kwa kweli ndiyo maana wanafanyiwa due diligence. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na swali la pili, nataka nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti hii ambayo tunaendelea nayo tumetenga fedha kwa ajili ya kuanza ama kuendelea na ujenzi pale tulipoishia ya Turiani – Mziha hadi Handeni kwa mwaka ujao wa fedha, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili licha ya majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inaweza ikanihakikishia kwamba wananchi wa Uchira, ambao nao walipisha ujenzi wa upanuzi wa barabara hii inayotoka Arusha – Moshi kwenda Holili, je, nao watalipwa chini ya mchakato huu ulioanza?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, lini sasa barabara hii itaendelezwa toka pale ilipoishia Tengeru, eneo la Arusha kuja Moshi, Himo mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba Mheshimiwa Dkt. Kimei kwa kweli suala la malipo ya fidia kwa hawa wananchi limekuwa ni suala ambalo kila tunapokutana na kuja ofiini analifwatilia, lakini tumelitolea majawabu na kwamba sasa tunakamilisha.

Mheshimiwa Spika, swali lake kuhusu wananchi ambao pia watapisha ujenzi, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kuwa tulifanya tathmini siku za nyuma, tutarudia ku-review zile tathmini ili ziendane na muda wa sasa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara ya Tengeru kuja huku Holili; JICA walishakubali, tumelijibu mara kadhaa, tutajenga hiyo barabara kwa kusaidiana na wenzetu wa Japan, ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Wananchi wa Jimbo la Nyang’hwale wanapenda kujua upembuzi yakinifu kuhusu barabara yao kutoka Kahama – Nyang’hwale mpaka Busisi, Sengerema utakamilika lini? Leo takribani miaka mwili tunaulizia jambo hili hatupati majibu, naomba majibu ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’hwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wiki iliyopita nilijibu pia hili swali. Hii barabara inahusisha mikoa takribani mitatu; Shinyanga, Geita na Mwanza. Upande wa Mwanza wanafanya Mkoa wa Mwanza, lakini kwa upande wa Shinyanga na Geita wanaosimamia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ni TANROADS Makao Makuu.

Mheshimiwa Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba walishakamilisha taratibu zote za kumpata Mhandisi Mshauri. Kwa hiyo, kazi inategemewa kuanza kwa sababu ni utekelezaji wa bajeti hii na wataendelea pia katika mwaka ujao wa fedha kuhakikisha kwamba wanakamilisha kuunganisha hiyo mikoa mitatu kupitia hiyo barabara aliyoitaja, ahsante.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Serikali, na kwa kuwa mradi huu umechukua miaka sita sasa tangu ulipositishwa, ninayo maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, je, ni lini sasa Serikali itakamilisha mchakato wa kupitia hasara zilizosababishwa na kusimamishwa kwa mkataba huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni lini Serikali itakamilisha mchakato wa kumpata mkandarasi mpya ili kazi ya ujenzi wa mradi wa Mhalala uweze kuanza? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyonyeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni Mashariki kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, suala la kwanza, Benki ya Maendeleo ya Ulaya iko tayari, na fedha zipo kwa ajili ya kuendeleza. Kilichokuwa kinachelewesha ni kwamba baada ya kuingia mgogoro wa kimkataba ilikuwa ni lazima Serikali ihakikishe kwamba wanakaa pamoja na mkandarasi huyu ili waweze kukamilisha changamoto zote zilizokuwepo, wakishakubaliana sasa ndiyo waingie mkataba kutafuta mkandarasi mwingine wa kukamilisha.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni imani ya Serikali kwamba kwa mwaka tunaoanza wa fedha tutahakikisha kwamba mkandarasi anapatikana, na kazi iliyobaki, Kituo cha Ukaguzi hiki cha Muhalala pamoja na kile cha Nyakanazi, kwa sababu vyote vilisimama kwa pamoja vinaanza kujengwa na kukamilika kwa sababu ni muhimu sana kwa ajili ya kulinda barabara zetu, ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niulize swali moja la nyongeza. Kwa sababu suala la ujenzi wa barabara tunatumia fedha nyingi na maeneo mengine mvua zimekuwa zikiharibu miundombinu hii, hii ni kwa sababu labda hatukufanya design au hatukufanya utafiti wa kutosha kwenye athari ya kimazingira. Je, ni nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba kabla ya ujenzi wa miundombinu hii ambayo inatumia gharama kubwa kuangalia athari za kimazingira zisilete matatizo katika miundombinu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara na hasa hizi za udongo na za changalawe mara nyingi zinaharibika hasa kipindi cha mvua na Serikali imekuwa ikitenga fedha nyingi kwa ajili ya kufanya ukarabati na hasa kutengeneza mitaro na mifereji ili kutoa hayo maji, kwa sababu moja ya chanzo kikubwa cha kuharibu barabara ni maji. Pia Serikali inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kutotumia barabara kwenye hifadhi za barabara na kupitisha mifugo kwenye barabara. Kwa sababu hicho pia ndiyo chanzo kikubwa cha kufanya uharibifu wa barabara, kwa sababu ukishalima karibu na barabara unatuamisha maji na hivyo barabara zinaharibika. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Barabara ya Kagoma – Biharamulo katika Mji wa Muleba pale, walielekeza maji kwenye makazi yatu ambapo wamechimba mtaro mkubwa ambao unajulikana kama Buhimba, lakini Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano wakati wa Kampeni 2020 - 2025 alitoa maelekezo mahususi kwamba Mamlaka zinazohusika wakae tumalize hilo tatizo: -

Je ni lini Mamlaka ya TANROADS itakuja kumaliza tatizo la maji katika eneo la Buhimba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sababu yalikuwa ni maelekezo mahususi na kuhusu eneo mahususi, naomba pia kutumia nafasi hii kumwelekeza Meneja wa Mkoa wa Kagera aende kwenye eneo lililokuwa limetolewa maelekezo na Mheshimiwa Rais, kutoa ama kuyatoa maji yaliyokuwa yameelekezwa kwenye makazi ya watu na kuyapitisha kwenye njia sahihi. Nimwombe atakapokuwa anafanya hivyo aweze kuwasiliana na Mheshimiwa Mbunge ambaye ametoa hoja hii, ahsante. (Makofi)

MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha inatuongezea pesa na wakandarasi zaidi ya mmoja, wawe watatu ili Barabara ya Mpanda – Kigoma ikamilike ili wananchi wa Mkoa wa Katavi waweze kufunguka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, mazungumzo hayo na Benki ya Afrika yatakamilika lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika taratibu za kandarasi inategemea na mlivyopanga lots ama vipande na vipande tunavyovijenga hakuna ambacho kwa sasa kinazidi kilometa 50.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo katika hivyo vipande vitatu vinavyojengwa kila kipande kina mkandarasi lakini tunategemea katika swali lake la pili kama African Development Bank tutakuwa tumekubaliana nao kutumia bakaa iliyobaki kukamilisha hiyo barabara kwa urefu wa kilometa 94 ni wazi kwamba hatutakuwa na mkandarasi mmoja tutakuwa na zaidi ya mkandarasi mmoja ili kukamilisha kazi kwa haraka kati ya Mpanda na Uvinza kwa kilometa 94 ambazo zimebaki, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara hii inaunganisha Mikoa miwili, Arusha na Manyara pia ni muhimu sana kwa uchumi wa Taifa. Sasa barabara hii kwa unyeti wake iko busy na imekuwa ni changamoto kubwa sana ya afya kwa wanachi walioko katika barabara hii kwa sababu ya vumbi. Naomba commitment ya Serikali kwamba; Je, ni lini ujenzi utaanza kwa sababu kuna fedha nyingi, kuna mpango wa RISE, kuna Agri - connect. Je, Serikali haiwezi ikafanya utaratibu barabara hiyo ianze kujengwa mara moja baada ya usanifu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kuna ahadi nyingi sana za Serikali, Viongozi Wakuu za ujenzi wa barabara kwa viwango vya lami, na mojawapo ni barabara ya King’ori kutoka Malula hadi Ngarenanyuki. Naomba niulize barabara ya King’ori kutoka Malula hadi Ngarenanyuki lini itajengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu ni ahadi ya Viongozi Wakuu wa Serikali. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, commitment ya Serikali imeshaonekana na ndiyo maana tayari tumeshaanza taratibu za kujenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami tukitambua kwamba inaenda kwenye sehemu muhimu sana ya kiuchumi eneo la mgodi wa Mererani lakini pia inaunganisha kama alivyosema Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Manyara. Isingekuwa rahisi kufanya chochote kabla ya kukamilisha usanifu. Kwa hiyo, kama fedha inaweza ikatokea yoyote katika kipindi hicho tutafanya, vinginevyo ni kwamba baada ya kukamilisha usanifu basi tutaipangia bajeti kwa mwaka ujao wa bajeti kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu hii barabara aliyoitaja. Ni kweli barabara ya King’ori – Ngarenanyuki ilikuwa inatengenezwa na wenzetu wa TARURA tumekasimiwa, kwa hiyo tunaendelea kutafuta fedha ili tuweze kuijenga hii barabara kwa kiwango cha lami kwa sababu inapita kwenye maeneo makubwa sana ya uzalishaji wa wenzetu ambao ndiyo wanalisha Mji wa Arusha. Ahsante.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mpango wa Serikali ni kuunganisha kwa kiwango cha lami kutoka Wilaya kwenda Mkoa. Waziri ni lini Serikali itaanza kujenga barabara Halmashauri ya Wilaya Mbogwe kwenda Geita Makao Makuu ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maganga Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli huo ndiyo mpango na bahati nzuri barabara alizozitaja Mheshimiwa Mbunge zitafadhiliwa na wenzetu wa World Bank kupitia mradi wa RISE ambao sasa hivi wanakamilisha kufanya review ya usanifu wa barabara za kuiunganisha Wilaya ya Mbogwe na Wilaya ya Geita kwa kiwango cha lami. Tunategemea kuanzia mwaka ujao wa fedha kwa sababu taratibu zinaendelea na ni fedha za World Bank, mara baada ya kukamilisha hizo taaratibu ujenzi utaanza kwa kiwango cha lami. Ahsante.

MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwanza ninaishukuru Serikali kwa kusaini mkataba wa Barabara ya Sengerema kwenda Nyehunge klilomita 54 lakini awali barabara ile ilisomeka Sengerema - Nyehunge na kipande cha Kahunda kilometa 32. Kilometa 32 za Nyehunge - Kahunda zimeondolewa.

Je, Serikali inaweza kutoa commitment ya kwamba kilometa 32 za Nyehunge - Kahunda pamoja na kipande cha Bukokwa – Nyakalilo zitajengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la, Mheshimiwa Mbunge Shigongo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii katika design, ili - design – wa kilometa zote mpaka hizo kilometa 32 kwenda Kahunda. Lakini tumeanza kuzijenga kulingana na upatikanaji wa bajeti na ndiyo maana commitment ya Serikali tayari tumeshasaini kipande hicho cha kilometa kuanzia Sengerema hadi Nyehunge kwa kuanzia na tukitegemea kwamba pengine katika mwaka wa fedha ujao, basi tutakamilisha hizo kilometa zote zilizobaki kwa sababu ndiyo mapango wa Serikali kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami. Ahsante.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Sengerema - Buchosa inaunganisha na Mkoa wa Geita kipande kidogo tu cha kilometa 14 kutoka Nyehunge kwenda Nzela, Serikali imeishia Nyehunge.

Je, Serikali ina mapango gani kuunganisha kutoka Nyehunge kwenda Nzela ambako Mheshimiwa Waziri unapita?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba tuna kila sababu ya kuunganisha Mkoa na Mkoa. Bahati nzuri hiyo barabara mimi nimeipita, kama nilivyosema kwamba mpango wa Serikali ni kuziunganisha Mkoa na Mkoa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, kadri fedha itakavyopatikana barabara hii ya kutoka Nyehunge hadi Nzela kipande kilichobaki pia kitajengwa kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na Nzela hadi Kome ambayo iko kwenye hatua za manunuzi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naishukuru Serikali vilevile kwa vile Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi amesharidhia hii barabara sasa hivi kuhudumiwa na TANROADS, lakini iko kwenye hali mbaya sana. Sasa je, ni lini barabara hii itaanza ujenzi ili irekebishwe kuanzia Mjele, Ikukwa na siyo Ikuwa mpaka Mlima Njiwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika hali hiyo ya barabara, barabara ya Haporoto – Ileya – Ishinda ambayo inahudumia wachimbaji wa Migodi ya Ileya na Ishinda, ni lini barabara hii itapata matengenezo kwa vile nayo iko kwenye hali mbaya sana? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema, baada ya kupandishwa hadhi hiyo barabara, TANROADS itaanza utekelezaji kwa bajeti ambayo tunaanza kuitekeleza kwa 2023/2024. Kwa hiyo kwa sasa wenzetu wa TARURA baada ya Juni watatukabidhi na sisi tutaanza utekelezaji huo kwa bajeti mpya, ahsante. (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kwa kuongezea tu kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa Ujenzi, barabara hii wakati bado ipo kwa TARURA ilikuwa imetengewa shilingi milioni 500 na Road Board kwa ajili ya matengenezo yake. Sasa baada ya kupandishwa hadhi fedha ile itahamia kwa wenzetu wa TANROADS ambapo bado watatekeleza kwenye barabara hii hii shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuijenga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili ya Barabara ya Haporoto – Ileya – Ishinda. Barabara hii ina urefu wa kilometa tisa na kweli nikiri kwamba kwa sasa hali yake si nzuri sana. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 ambao tunauanza mwezi unaofuata, tayari barabara hii imetengewa shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuweza kutengeneza yale maeneo korofi kwa kumwaga changarawe na kuhakikisha kwamba inapitika vizuri, kwa sababu inaelekea katika eneo ambalo lina machimbo. Kwa hiyo nimtoe hofu Mheshimiwa Njeza, kwamba muda si mrefu ataona utekelezaji wa matengenezo ya barabara hii kwa hizi kilometa tisa.
MHE. FURAHA M. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ukerewe ni kisiwa na kwenye bajeti ya mwaka huu Serikali imetenga fedha ya kujenga barabara hiyo ya kutoka Kisorya kwenda Nansio. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Matondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli dhamira ya Serikali ni kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Mbunge atakubaliana na mimi kwamba tayari tumeshajenga sehemu kubwa ya hiyo barabara. Hela iliyotengwa ilikuwa kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa daraja ambalo lina kilometa takribani moja, lakini kwa maombi ya wana Ukerewe na Mheshimiwa Mbunge wa Ukerewe, wameomba badala ya kuanza daraja kwa kuwa tunavyo vivuko viwili vikubwa ambavyo vitaendela kufanya kazi na hasa baada ya kuongeza kivuko kipya ni bora tukajenga barabara ya lami kuanzia Lugenzi hadi Nansio na wakati Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi anawasilisha bajeti alitoa commitment kwamba tutaanza kujenga mwaka ujao wa fedha barabara hii kwa kiwango cha lami kuanzia Nansio kuja Lugezi. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais mwaka jana iliahidiwa kujengwa barabara kutoka Mafinga inayokwenda Madibila kupitia Sadani.

Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli swali hili limeulizwa jana na Mheshimiwa nakumbuka wa Mbarali na nilijibu kwamba tutaendelea kulitengeneza, lakini marekebisho tu ni kwamba, kama alivyosema wakati Mheshimiwa Rais ametembelea Mkoa wa Iringa, Wabunge wa Mkoa wa Iringa hasa Wilaya ya Mufindi waliomba barabara hiyo ijengwe kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Rais alitoa ahadi na akatoa maelekezo na Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi akiwepo, ameshatoa maelekezo, kwamba ile ahadi ya Rais ianze kutekelezwa mwaka huu. Kwa hiyo, tutaanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami kama maagizo ya Mheshimiwa Rais yalivyotolewa kuanzia huku Mafinga kwenda Mbarali, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami kipande cha barabara kinachoanzia Ngarenanyuki hadi Oldonyo Sambu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja inachangiwa kipande na barabara yetu ya TANROADS, pia kuna kipande ambacho wenzetu wa TARURA wanakifanya. Kwa upande wetu wa TANROADS tayari tumeshafanya usanifu na tunachofanya sasa hivi ni kuhakikisha kwamba hii barabara inapitika kwa muda wote wakati tukiendelea kutafuta fedha ili kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Kokoto mpaka Mwandege ndiyo lango kuu la magari yanayotoka Kusini. Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua barabara hiyo ili kupunguza msongamano?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika bajeti ambayo tumeitenga mwaka ujao na kweli nakubaliana kuna changamoto kubwa sana. Pale ambapo BRT II inaishia mwaka ujao tunaanza kutekeleza mradi wa kujenga kilometa 3.8 kwa barabara hizo nne, lakini mpango ni kwenda mpaka Vikindu kwa ajili ya kujenga hizo barabara nne kupunguza changamoto ya msongamano wa hizo barabara.
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza na ni kwamba zimebakia siku nane leo kabla ya mwaka wa Serikali kuisha na Serikali ilikuwa imetueleza kwamba Sengerema tutafanya usanifu barabara ya Sengerema - Ngoma na Busisi - Ngoma kwa ajili ya lami kwenda Nyangh’wale na zimebakia siku nane hatujaona mkandarasi, Nini kauli ya Serikali Mheshimiwa Waziri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii kwa sababu inaunganisha mikoa miwili wa Geita na Sengerema Mkoa wa Geita na Mkoa wa Mwanza sehemu kubwa inasimamiwa na Makao Makuu ya TANROADS ninataka nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Mhandisi Mshauri ameshapatikana kwa ajili ya kuanza kazi hii ya usanifu wa hii barabara.

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, tuna barabara inayounganisha Mikoa ya Kagera na Geita kutokea Katoke – Buharamulo kwenda kwenye Bandari ya Nyamirembe, na tuliahidiwa kwamba ingeanza kufanyiwa ujenzi mwaka huu wa fedha. Sasa tunaelekea ni mwezi wa tano sasa hivi imebaki miezi miwili hatujaona mkandarasi site.

Ni lini sasa barabara hii itaanziwa ujenzi ili wananchi wale waweze kuanza kuitumia ikiwa katika kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, barabara ya Nyamirembe – Katoke inatoka kwenye Bandari ya Nyamirembe ambayo tayari imeshakamilishwa na lengo ni kuunganisha hii bandari na Biharamulo. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ipo kwenye mpango na imeshaombewa kibali ili iweze kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi, naomba kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ni lini barabara ya kutoka Bukombe kuja Katoro yenye urefu wa kilometa 65 itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? Maana ni siku nyingi iliahidiwa.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja inatekelezwa kwa mradi wa Rais, na taratibu zipo zinaendelea kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Nduguti – Iguguno yenye urefu wa kilometa 42 inayopita Makao Makuu ya Wilaya ya Mkalama kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aysharose Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum - Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mattembe kwa kufuatilia miundombinu ya Mkoa wa Singida. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama ilivyo kwenye Ilani ya CCM barabara hii itaanza kufanyiwa usanifu wa kina na kukamilisha mwaka unaokuja wa fedha ikiwa ni maandalizi ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea yenye kilometa 45 upembuzi yakinifu na wa kina umefanyika zaidi ya miaka tisa iliyopita. Ni lini Serikali itaanza ujenzi sasa barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chinguile, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ambayo inaunganisha Wilaya ya Masasi na Wilaya ya Nachingwea, kwa maana ya Mikoa wa Mtwara na Lindi, ni muhimu sana. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii kama bajeti ambayo tunategemea kuiwasilisha wiki ijayo itapita, ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)

MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali iliahidi kufanya upembuzi yakinifu wa barabara ya milimani ya Mwembe – Mbaga – Mamba – Ndungu ili iweze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Je, barabara hii ya Mwembe – Mbaga ya milimani ni lini itatengewa fedha kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu kwa ajili ya kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi barabara hii mimi tayari nimeshaitembelea na kuiona na kuona changamoto zake. Moja ya vitu ambavyo Serikali tunavifanya kwa nature ya barabara yake, tumemuagiza Meneja wa TANROADS hata kabla ya kuanza kufikiria kuijenga yote kwa kiwnago cha lami, aainishe maeneo yote korofi ambayo kipindi cha masika hayapitiki ili Serikali iweze kuyajenga na kuhakikisha kwamba mwaka wote barabara hii inapitika. Lakini taratibu zipo kwa ajili ya kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara yote aliyoitaja ya Mwamba – Miamba – Ndungu ili kufanya maandalizi kwa ujenzi kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yana dhamira njema ya kuunganisha Mikoa ya Singida na Mbeya kwa barabara ya kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa maelezo yake Mheshimiwa Naibu Waziri; ni lini sasa huyu mkandarasi atafika Itigi ili wananchi nao waanze kufurahia matunda mazuri ya nchi yao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mkoa wa Singida unaunganishwa na Mkoa wa Simiyu kwa barabara ya vumbi kupitia Daraja la Sibiti. Je, ni lini sasa na barabara hii nayo itaweza kuanza ujenzi wa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo: -
Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali inapokea pongezi za Mheshimiwa Mbunge kwa kuanza ujenzi wa barabara hii. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati nakuja hapa Bungeni tayari mkandarasi wako wanasainiana mkataba na mara baada ya kufanya kazi hii naamini mkandarasi ataanza kukusanya vifaa ili kuweza kwenda kuanza hii kazi. Kwa sababu baada ya kusaini mkataba kazi inayofuata ni mobilization na kuanza kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake la pili la kuunganisha Mkoa wa Singida na Simiyu; barabara hii aliyoitaja ambayo inapita Daraja la Sibiti tayari imeshakamilishwa kwa kufanyiwa usanifu wa kina. Daraja limeshajengwa; nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pia kwamba katika mwaka huu wa fedha tumeongeza kilometa za kujenga barabara za lami ambazo zinaingia kwenye Daraja la Sibiti mpaka kilometa 25. Na Serikali katika bajeti inayokuja nina hakika tutaanza kwa awamu kujenga vipande vya barabara za lami ili kuunganisha Mikoa ya Singida na Simiyu kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa barabara ya Makambako – Songea ni mbovu na nyembamba sana na hivi juzi imeleta ajali na watu tisa wamefariki.

Je, lini Serikali itatengeneza barabara hii kwa kiwango cha lami yenye ubora kutoka Makambo mpaka Songea? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Njombe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa kwamba barabara ya Makambako – Njombe hadi Songea ni barabara ambayo kwa kweli imechoka, ni barabara ya zamani sana, barabara ya tangu miaka ya 1984. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii tayari usanifu ulishakamilika na World Bank wameshaonesha nia ya kuijenga barabara hii upya ikiwa ni pamoja na kuipanua kwenye viwango vya sasa na mradi huu utahusisha pia na kujenga barabara ya bypass katika Mji wa Songea. Ahsante.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa fursa ya swali la nyongeza.

Mchakato wa mkandarasi wa kujenga barabara ya Ntendo – Muze imechukua muda mrefu takribani miezi 11 mpaka sasa. Nataka kujua ni lini mkandarasi anaripoti site kuanza ujenzi wa lami katika barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deus Sangu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Ntendo – Muze – Kiliamatundu ina package mbili; mkandarasi tayari ameshasaini kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami kilometa za awali na kilometa zingine zinazoongezeka zipo kwenye taratibu za manunuzi. Kwa hiyo, muda wowote nataka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge mkandarasi atakuwa site kwa ajili ya kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. SANTIEL E. KIRUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Je, kutokana na viwanja vingi vya Serikali kujengwa na makampuni ya nje. Nini kauli ya Serikali kuwajengea uwezo makampuni ya ndani ili yaweze kujenga viwanja hivi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kutokana na mkataba huu kusainiwa tangu umesainiwa ni miaka Mitano. Nini kauli ya Serikali itawalipa fidia lini hawa wananchi wa Shinyanga kwa sababu tangu mwaka 2017 mpaka sasa 2022 miaka mitano imepita, itawalipa fidia ya mwaka 2017 au mwaka 2022, kutokana na bidhaa nyingi kupanda?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Santiel Eric Kirumba, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Shinyanga, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninampongeza Mheshimiwa Mbunge Santiel kwa jinsi anavyofuatilia ujenzi wa uwanja huu. Suala la Wakandarasi wa ndani. Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imekuwa mara kwa mara ikihimiza na ikiwajengea uwezo Wakandarasi wote wa Tanzania ili waweze kufanya miradi mikubwa. Hii siyo tu kwa viwanja vya ndege ni pamoja na miundombinu mingine ikiwemo majengo makubwa na hata barabara. Kwa hiyo, kinachofanyika kwanza ni kuwapa elimu ya kuwaunganisha pamoja ili waweze kuwa na mitaji mikubwa pia kuwawezesha ili waweze kupata mikopo kwa taasisi mbalimbali za fedha ikiwemo mabenki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ipo inafanya kazi hiyo na tunaamini kwa kuwawezesha Wakandarasi wa ndani maana yake fedha yetu nyingi itaendelea kubaki na kukuza uchumi pia kuwezesha uwezo wa hawa Makandarasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili kuhusu fidia. Serikali ilikwishawalipa fidia wananchi ambao wamepisha ujenzi. Kwa mujibu wa sheria zetu tunapolipa fidia tunaondoa kitu kinachoitwa uchakavu na hasa uchakavu wa majengo. Masharti ya wenzetu hawa ambao wanatoa fedha wana sharti moja kwamba ni lazima fedha ya uchakavu pia ilipwe. Kwa hiyo, Serikali imeshafanya tathmini ya uchakavu wa yale majengo na tayari yameshawasilishwa Wizara ya Fedha ili wakalipwe zile fidia za nyongeza kwa uchakavu wa yale majengo. Kwa hiyo, tayari tuko kwenye process na hawa watu wataongezwa fidia kwa maana ya ile ambayo sheria yetu ilikuwa inasema tusiwalipe lakini wanaotufadhili wanatuambia ni lazima pia walipwe. Kwa hiyo wananchi hawa watapata nyongeza ya fidia tofauti na waliyopata ile ya awali. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Je, Serikali itamaliza lini uwanja wetu wa ndege wa Iringa, kwa sababu uwanja ule tunategemea sasa hivi Mama amehamasisha royal tour kwa ajili ya utalii mkubwa katika hkivutio cha Ruaha na vivutio vingine vilivyoko katika Mkoa wa Iringa na Nyanda za Juu Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba ujenzi huu unaendelea. Serikali inaendelea kuujenga uwanja huu na Wakandarasi wako site. Pengine tu ni kuwahimiza Wakandarasi waweze kuongeza speed na tunajenga kwa fedha ya Serikali pia wenzetu wa World Bank wameonesha utayari wa kuweza kusaidia ili kukamilisha ujenzi wa uwanja huu ili kuweza kuimarisha shughuli za utalii ambazo tayari Mheshimiwa Rais ameshakuwa champion wa hiyo kazi. Kwa hiyo tunakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba uwanja huu tutaukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, toka mwaka jana kwenye bajeti majibu ya Serikali yamekuwa ni haya haya hayabadiliki. Hatua za mwisho za kusaini mkataba. Swali langu la msingi lilikuwa ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ipi Barabara ya Handeni - Kwa Magome, Nziha - Turiani. Ni lini Serikali pia itaanza kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Reuben kwa jinsi anavyofuatilia barabara ambazo zinaanzia katika Jimbo lake kwenda kwenye Majimbo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyoongea nataka nimhakikishie Mheshimiwa Reuben kwamba tayari kazi ya ujenzi imeshaanza na hivi tunavyoingia huku Mkandarasi ameshapatikana na sasa ameanza mobilization kupeleka vifaa site kwa hizo kilomita 20 ambazo zilishatangazwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya kutoka Handeni Mjini kuja Turiani naomba tusubiri bajeti ipitishwe halafu tuone tutakachofanya katika hiyo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; kumekuwa na malalamiko kwa wananchi kadha wa kadha ambayo bado wanaonesha namna gani ambavyo hawakupata stahiki hizo.

Ninaomba kujua ni lini Mheshimiwa Waziri utatenga muda ukawasikilize wananchi wale ili uweze kupata ufumbuzi wa malalamiko hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Assa Nelson Makanika, Mbunge wa Kigoma Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba nipo tayari kwenda kuwasikiliza wananchi, lakini pia nitaomba tukubaliane naye mara baada ya Bunge hili muda sahihi na maeneo ambayo atataka Mheshimiwa Mbunge twende tukawasilize wananchi hawa ili tuweze kutatua hii changamoto ya fidia ambayo ni ya muda mrefu sana. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, barabara ya Machine Tools kwenda Kialia Machame Girls ilijengwa mwaka 1930 kwa sheria ya mkoloni, lakini mwaka 2004 wananchi waliwekewa alama ya “X” nyumba zao wakarudia tena mwaka 2007.

Swali langu, je, ni lini Serikali italipa fidia wananchi ambao waliwekewa alama ya “X”?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, niwajibu na jukumu la Serikali kabla ya kuanza ujenzi wowote wa barabara kuhakikisha kwamba inalipa fidia; na kwa kuwa suala hili ni la muda mrefu mwaka 2004 - 2007 tunaongelea miaka kama 18 hivi. Kwa hiyo, nitamuomba Mheshimiwa Mbunge na nitoe agizo kwa Watendaji wa Wizara kutafuta documents zinazohusu barabara hii ili tuweze kukubaliana na Mheshimiwa Mbunge pia tuweze kwenda eneo hilo la barabara aliyoainisha kuongea na wananchi tuone tatizo ni nini ambapo mpaka sasa hivi hawajalipwa fidia hiyo. Ahsante.

MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, wananchi waliokuwa pembeni ya barabara inayotoka Kongowe mpaka Kokoto wamefanyiwa uthamini zaidi ya miaka mitatu sasa.

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia wananchi hao ili kupisha ujenzi wa barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Chaurembo, Mbunge wa Mbagala kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Mbagala ambao wamewekewa alama ya kupisha eneo hili la mradi huu kwamba kabla ya kuanza ujenzi Serikali itahakikisha inawalipa fidia yao. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha kwanza kuanza kwa ujenzi na kuwalipa hao wananchi fidia yao. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa Mwenyezi Mungu amefungua neema katika Wilaya ya Nyang’ahwale kuwa na machimbo mengi sana ya dhahabu na kuwa kuna mzunguko mkubwa wa kiuchumi ikiwemo ongezeko la vipando vya magari pamoja na pikipiki; pamekuwa panapitika magari zaidi ya elfu moja kwenye makao makuu ya wilaya na kutimua vumbi jingi. Kwa kuwa Serikali imesema itajenga hizo kilometa mbili; je, ni lini kwa kauli ya Serikali ujenzi huo utaanza?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; niishukuru Serikali kwa kuweka mpango wa kujenga kilometa 123 kwa kiwango cha lami kutoka Nyankumbu – Nyalubele – Ijundu – Kharumwa - Bukwimba mpaka Nyang’holongo. Je, ni lini sasa ujenzi huo utaanza? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Nyang’hwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kilometa hizo mbili ni sehemu ya hiyo barabara ambayo tunategemea kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili baada ya kukamilisha tuweze kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, ni lini tutaanza ni pale ambapo tutakamilisha hatua za awali za kuifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa ni hatua za awali baada ya hapo tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza na naishukuru Serikali kwa Wizara ya Ujenzi kwa kuhangaika na ujenzi wa lami kwa barabara ya Bariri - Mgeta. Sasa kwa sababu mmekwishafanya upembuzi yakinifu na mmeshafanya tathimini ya ujenzi; ni lini sasa hii barabara ya Mgeta - Bariri itajengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Bariri - Mgeta ni barabara ambayo inasimamiwa na Wakala wa Barabara (TANROADS) naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili ikishapata fedha basi hii barabara ambayo ni njia ya mkato kwenda Nata - Mgumu iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa vile ujenzi wa barabara ya Chekereni – Kahe - Mabogiri kwa kiwango cha lami ipo kwenye Ilani ya CCM na pia ni ahadi ya viongozi wakubwa wa kitaifa. Je, ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimei, Mbunge wa Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoainisha iPo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika kipindi hiki kuna hatua ambazo tutaanza kuzitekeleza kama tulivyoainisha kwenye Ilani lakini itategemea sana na kadri ya fedha itakavyopatikana. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Je, Serikali lini itakamilisha kujenga barabara ya Kibamba - Kibwegere mpaka Mabwepande kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, Dar es Salaam kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ipo kwenye mpango wetu kati ya barabara ambazo zipo Dar es Salaam kwa ajili ya kupunguza misongamano ya Dar es Salaam. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami ikiwa pia ni mkakati wa kupunguza foleni kubwa zinazotokea katika Jiji la Dar es Salaam. Ahsante.

MHE. ANATROPIA L. THEOENEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; barabara ya Benako kuja Karagwe haina lami na hii ni barabara muhimu sana kwa sababu ya ulinzi, kule kuna utekajeji lakini pia ufanyaji wa biashara kati ya Tanzania na Rwanda. Swali ni lini hiyo barabara itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ambayo inaanzia Bugene kupitia Chato hadi Benako ni barabara ambayo inaunganisha pia na nchi yetu Uganda nchi yetu, lakini pia kwenda Rwanda. Barabara hii ipo mbioni kuanza kujengwa kilometa 62 kwa kiwango cha lami na ipo kwenye mpango kuanzia mwaka huu wa bajeti. Ahsante. (Makofi)

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ni lini Serikali itajenga Daraja la Itunundu kwenda Igodikafu Jimbo la Isimani ambako wananchi wanapata shida sana hasa wakati wa masika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba daraja alilolitaja litajengwa kama lilivyoainishwa kwenye ilani na hasa baada ya kufanyiwa usanifu wa kina.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika majibu ya Naibu Waziri amesema wako kwenye hatua za mwisho kwenda kusaini mkataba wa ujenzi wa daraja hilo: Nataka kujua je, ni lini hasa mkataba huo unatarajiwa kusainiwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili: Kwa kuwa ujenzi wa daraja la Bweni Pangani unakwenda sambamba na ujenzi wa barabara ya Tanga - Pangani kilometa 50; na kwa kuwa ujenzi wa barabara hiyo uko asilimia 37: Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kuwa daraja hilo litakwenda kukamilika kwa wakati baada ya mkataba huo kusainiwa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamilu Zodo, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba muda wowote kabla ya mwisho wa mwezi huu tuna uhakika mkataba huu utakuwa umesainiwa na daraja hili ujenzi wake unafadhiliwa na Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia barabara aliyoitaja tuna uhakika itakwenda sambamba na ndiyo maana kwa sababu ya ukubwa wa hili daraja ilipewa lot yake, ni barabara ambayo inajitegemea, ina lot yake. Kwa hiyo, tuna uhakika kwa kuwa ina lot yake na mkandarasi atakayekuwa amepatikana atasimamia hilo daraja tu na barabara za maungio wakati mkandarasi mwingine anaendelea kujenga barabara, kwa hiyo, tuna uhakika wakati mkandarasi anakamilisha barabara, daraja pia litakuwa linakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa hii nafasi. Katika Jimbo la Manyoni Mashariki, tuna araja la Sanza ambalo tayari upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishafanyika na hilo daraja liliingizwa kwenye bajeti hii inayoishia. Sasa nini kauli ya Serikali kwamba ni lini ujenzi wa hili daraja utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Chaya, Mbunge wa Manyoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, daraja hili ni kati ya madaraja makubwa ambayo yameainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, nasi kama Wizara, daraja hili tayari limeshapata kibali cha kuanza kujengwa pamoja na barabara zake za maingilio.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza. Wizara ya Ujenzi kupitia TANROADS ilitenga Shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Sangatini eneo la Tundwi Songani kule Pemba Mnazi katika mwaka wa fedha 2021/2022 hadi sasa ujenzi ule haujaanza: Ni lini ujenzi wa daraja Sangatini utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Daraja la Sangatini lilishatengewa fedha na fedha ipo. Tender ilitangazwa lakini ali-tender mtu mmoja na akawa ame-tender bei ya juu na tumeshalitangaza tena. Nataka nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tender zitafunguliwa wiki hii na baada ya hapo daraja hili litaanza kujengwa kwa bajeti ya mwaka huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mheshimiwa Waziri amenijibu mchakato. Najua na ninatambua taratibu kwamba lazima hiyo michakato ifanyike. Sasa swali langu linabaki, ni lini? Kwa sababu natambua mtatangaza zabuni na Serikali inafuata utaratibu na schedule; kwa hiyo, nataka kujua ni lini? Hilo ni swali la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Wilaya ya Kyerwa, TANROADS ina mtandao mdogo wa barabara ya Kyerwa na TARURA wana mzigo mkubwa ikiwepo na madaraja: Je, Serikali haioni ni wakati muhimu wa kutanua mtandao wa barabara kuunganisha Kata ya Nkwenda - Songambele pamoja na Karagwe na Rwanda kwa upande wa Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, huu tena siyo mchakato, tumetaja tarehe 10 mwezi huu wa Tano, zabuni imefunguliwa. Ukishafungua zabuni, maana yake tayari unaanza kujenga utakapokuwa umempitisha Mkandarasi baada ya kufanya evaluation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali lake la pili, zipo taratibu ambazo zinafuatwa ili barabara zipandishwe kutoka hadhi ya kuhudumiwa na TARURA na kuhudumiwa na TANROADS. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba viko vikao ambavyo vinapitia, zinaletwa kwenye Wizara, Wizara inaenda kufanya tathmini na kuona hizi barabara zinakidhi vigezo halafu zinapandishwa kutoka TARURA kuja TANROADS? Ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Je, Serikali lini itajenga kwa kiwango cha lami barabara ya kutoka Kibada, Kisarawe II mpaka Tundi- Songani?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Mariam Kisangi Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti iliyopitisha jana barabara hiyo inajengwa kwa kiwango cha lami na iko kwenye manunuzi na tutajenga kilomita 41 kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ANTHONY A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini barabara inayoanzia KK Kata ya Kimo ikipitia Ikwenjola, Ikuti, Ibungu mpaka Kafwafwa ambayo iko kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantona Mbunge wa Rungwe Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Kimo, Kafwafwa, Luswiswi, Katengele hadi Ibunge kwenye bajeti ya mwaka huu tunaokwenda kuitekeleza imepangwa ifanyiwe upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ikiwa na maandalizi ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami baada ya kukamilisha hizo taratibu za awali, ahsante.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, kwa kipindi kirefu kumekuwa na mchakato wa upanuzi wa barabara ya New Bagamoyo Road na Old Baganoyo Road kwa ajili ya kuondoa foleni Mkoa wa Dar es Salaam. Na kwenye New Bagamoyo Road hususan kutoka Tegeta Kibaoni kwenda mpaka Daraja la Bagamoyo. Na kwa Old Bagamoyo Road kutoka Morocco mpaka Afrikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nilitaka nijue ni lini mchakato huu utaanza kwa sababu imekuwa kwenye mipango muda mrefu na utekelezaji umekuwa finyu. Ni lini barabara hizi mbili zitapanuliwa New Bagamoyo Road kwenye eneo ambalo nimekutajia na Old Bagamoyo Road katika Ukanda wa Morocco Daraja la Mlalakua mpaka Afrikana?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mpango kabambe wa kupunguza misongamano kwenye miji na ikiwepo Mji wa Dar es Salaam. Kwa hiyo, katika bajeti tunazoenda nazo barabara hizi zimeainishwa kwamba itakuwa ni barabara ambazo zitapewa kipaumbele ili kujengwa kwa barabara nne ama sita ili kupunguza msongamano. Kwa hiyo, nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taratibu zipo zinaendelea na fedha itakapopatikana basi hiyo kazi itaanza mara moja.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ni lini Serikali itapasua na kumalizia barabara inayotoka Mtowisa, Ngongo mpaka Kristo Mfalme Sumbawanga DC? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY KASEKENYA MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum Rukwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara aliyoitaja pia ni ahadi ya viongozi wa kitaifa. Naomba nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili kuweza kuipasua hii barabara inayoanzia Mtowisa kama ambavyo viongozi waliahidi kufanya hivyo, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa uwanja wa Mtwara inawezekana tukauita international airport kwa sasa package yake ya mradi ule ulikuwa ni kuwepo na gari ya zimamoto nikimaanisha fire. Je, ni lini sasa Wizara itahakikisha kwamba mkandarasi anatuletea gari ya zimamoto pale airport?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili uwanja wa airport umepakana na maeneo ya wananchi, lakini baadhi ya maeneo ya wananchi lilipita bomba la gesi na wananchi wale wakalipwa. Sasa ni lini Serikali itaamua kuwalipa wananchi ambao bado hawajalipwa ili waondokane na adha hiyo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini kama ifuatavyo:-

Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika ukarabati na upanuzi wa uwanja huu suala la gari la zimamoto ni sehemu ya mradi huu na tayari mkandarasi ameshatoa order gari itanunuliwa kutoka Ujerumani na thamani yake itakuwa ni bilioni 1.4. Kwa hiyo tayari gari limeshaanza kutengenezwa kwa ajilli ya uwanja wa Mtwara, ahsante.
MHE. NORAH W. MZERU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante ni upi sasa mkakati wa Serikali wa kujenga barabara zote za Morogoro ili ziweze kupitika msimu mzima?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE). Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba baabara zote za Mkoa wa Morogoro zinapitika ni pamoja na kuzijenga zile ambazo tumeziainisha kwa kiwango cha lami, lakini pia kuzitengea fedha barabara zote kwa ajili ya ukarabati na kuna barabara ambazo tayari zipo kwenye kutangazwa kwa ajili ya kuzijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ni kuhakikisha barabara zote zinapitika mwaka mzima, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia ametangaza kwa nguvu kubwa utalii kupitia Royal Tour na kwa kuwa barabara zinazokwenda katika Mbuga za Wanyama kama Ruaha National Park hadi leo hazijajengwa kwa kiwango cha lami.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara zote zinazokwenda katika mbuga za wanyama zinajengwa kwa kiwango cha lami ili watalii watakapokuja tutendewe haki na Nyanda za Juu Kusini tupate watalii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Iringa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa kuanza na barabara ya Iringa kwenda Ruaha National Park, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara hiyo, lakini pia Benki ya Dunia (World Bank) imeonesha nia ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa maana ya barabara zote zinazoenda kwenye mbuga kama ukipitia kwenye kitabu chetu cha bajeti barabara nyingi zinazokwenda kwenye mbuga zimefikiriwa na kutengewa fedha ili kuboresha sekta hii ya utalii ambayo Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan tumeona jinsi ambavyo amefanya kwenye Royal Tour kwa hiyo na sisi hatutamwangusha kuhakikisha kwamba tunatengeneza miundombinu bora kwa ajili ya watalii kwenda kwenye mbunga za wanyama, ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kuuliza ni lini barabara ya Kolandoto kwenda Mwangongo yenye kilometa 63 itaanza utekelezaji kwasababu mwaka huu wa fedha imetengewa bajeti ya fedha shilingi 2,000,000,000? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Butondo, Mbunge wa Kishapu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii tumeiweka kwenye mpango kwa ajili ya kuanza ujenzi kwa kiwango la lami kuanzia Kolandoto hadi Lalago na Lalago hadi Mwanuzi kilometa hizi 62 na kilometa 60 katika mwaka huu wa fedha, ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ya kutokea Namtumbo kwa maana ya Lumecha, Kitanda, Londo, Malinyi, Kilosa kwa Mpepo hadi Lupilo wakati Mheshimiwa Waziri anajibu hoja za Wabunge kwenye hotuba yake alisema imeingizwa au imeorodheshwa katika mpango wa EPC, something like that ambao utahusisha wajenzi binafsi.

Mheshimiwa Naibu Waziri unaweza ukawaeleza vizuri wananchi wa maeneo hayo hususani wananchi wa Namtumbo na Malinyi kwa sababu hawakuelewa vizuri mpango huu ukoje ili wajue barabara hii itajengwa na mpango huu lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye jibu langu la msingi kwanza tutakuwa na mpango wa muda mfupi kuhakikisha kwamba tunaainisha maeneo muhimu korofi tuweze kuyakarabati ili barabara hii ipitike kwa muda wote, lakini kwa suala la EPC+F kwa maana ya Engineering Procurement Construction and Financing, ni suala ambalo litahitaji muda. Nitamuomba Mheshimiwa Vita Kawawa kama ataweza akatuletea swali la msingi ama tutakutana naye ili kuweza kulielezea kwa mapana na marefu kwa ajili ya kutoa uelewa kwa Waheshimiwa Wabunge wote, ahsante.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri yenye kutia matumaini kwenye hizi kata ambazo kwa kweli zina changamoto kubwa ya mawasiliano.

Je, niombe kupata commitment ya Serikali ni lini sasa kama zimetiwa kwenye mpango, ujenzi wa minara hii utafanyika kwa ajili ya hizo kata tajwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE) K.n.y. WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, napenda kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu la msingi minara hii itaanza kujengwa kwa mujibu wa sheria kwa kuwa tutatangaza kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha huu, kwa hiyo, tunaamini mchakato umeshaanza na mara mzabuni atakapoanza basi minara hii itaanza kujengwa kufuata na taratibu za manunuzi ahsante.
MHE. REUBEN N. KWAGILWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kwenye swali hili.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni lini sasa Serikali itamkabidhi mkandarasi huyu site ili ujenzi uweze kuanza mara moja? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza; barabara ya Handeni – Mziha – Turiani ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka karibia 30.

Je, Serikali haioni kwamba inakikosea Chama cha Mapinduzi kwa kutotekeleza ahadi yake ambayo ipo kwenye Ilani kwa miaka 30 iliyopita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii kama nilivyosema kwenye jibu la msingi mkandarasi ameshasaini tangu tarehe 11 Aprili na anaitwa Hernan Highway Engineering Group Company Limited na sasa hivi anachofanya ni maandalizi kwa ajili ya kuanza ujenzi. Kwa hiyo, taratibu zitakapokamilika ili akamilishe site tutamkabidhi na tutapenda kwa kweli Mheshimiwa Mbunge aweze kuwepo wakati sasa anaanza kazi rasmi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu barabara ya Magole – Mziha – Handeni; Serikali imeeshaanza kwa kipande cha Magole – Turiani na katika mwaka huu wa fedha, fedha imetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa barabara hii ikiwa ni utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi lakini pia kuhakikisha kwamba hii barabara tunaijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kutoka Masasi – Nachingwea kuelekea Liwale kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Pathan, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Lindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea kwenda Liwale Serikali imetenga bajeti kwenye bajeti ambayo imepitishwa kuanza na eneo la Masasi kwenda Nachingwea. Kwa hiyo, barabara hiyo tuna hakika itaanza utekelezaji kwa kiwango cha lami kwa mwaka fedha tunaoenda kuuanza sasa. Ahsante.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kupata nafasi.

Nilitaka kujua ni lini Serikali itatafuta fedha kwaajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Amkeni – Kitangali kwenda Mtama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ina azma ya kujenga barabara zote kwa kiwango cha lami lakini kinachotegemea ni upatikanaji wa fedha na bajeti itakavyoruhusu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri fedha itakavyopatikana barabara hii pia itaingizwa kwenye mpango ya kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya kutoka Kilosa – Ulaya kwenda Mikumi ambayo inapitia Masanze - Zombo na Ulaya ni barabara muhimu sana kwa kuchukua watalii kutoka SGR Station pale Kilosa kuja Mikumi mbugani na barabara hii ipo kwenye Ilani ya Uchaguzi ya mwaka 2010, 2015 na 2020.

Sasa kwa kuwa mimi siwezi kuruka sarakasi, nifanye nini ili Serikali ijue kwamba barabara hii ni muhimu kutengenezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara hii ilishaanza kujengwa ila bado haijakamilika nani azma ya Serikali kuikamilisha barabara hii na ni barabara ambayo inaunganishwa na barabara ya Mikumi – Kidatu hadi kwenda Songea.

Kwa hiyo, katika mipango ambayo Serikali inaendelea nayo kama alivyowasilisha Mheshimiwa Waziri wakati wa bajeti barabara ambazo zinafikiriwa pengine kujengwa kwa mpango wa EPC ili kuikamilisha barabara yote. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu ya kuridhisha.

Kwa kuwa barabara nyingi hapa nchini zimeshafanyiwa upembuzi yakinifu kwa muda mrefu sasa na hizo barabara zimeshakuwa ni nyingi sana; na bado ukiuliza unaambiwa tunatafuta fedha kwa ajili ujenzi.

Je, Serikali haioni kwamba imefika wakati sasa tusitishe kwanza kuendelea kufanyia upembuzi yakinifu tumalize hizi barabara ambazo tayari zimeshajengwa ili resource tulizonazo tumalizie hizi zilizojengwa ndipo tuendee kufanya upembuzi yakinifu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, iko barabara inayotoka Masasi kwenda Nachingwea mpaka Liwale zaidi ya kilometa 158, barabara hii imeshafanyiwa upembuzi yakinifu zaidi ya miaka minane sasa.

Je, ni lini Serikali wataijenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ni maelekezo ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi kuzifanyia upembuzi yakinifu na usanifu wa kina barabara ambazo tunaendelea nazo. Lakini pia naomba nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba moja ya mahitaji ili barabara ziweze kujengwa kwa kiwango cha lami ni kujua gharama zake ili hata wakati Serikali inatafuta fedha inakuwa inafahamu gharama ya zile barabara, inakuwa inafahamu ni wananchi gani ambao watapisha ujenzi, lakini pia inasadia kuzuia wananchi wasijenge maeneo ambako barabara itapita.

Kwa hiyo, tutaendelea kufanya usanifu ili kuwa tayari tunapopata fedha tuanze kujenga badala ya kusubiri kuanza usanifu pale tunapokuwa tumepata fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali lake la pili, barabara aliyoitaja ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale, katika bajeti hii tumetenga fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga barabara kuanzia Masasi kwenda Nachingwea na Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili kipande cha Nachingwea kwenda Liwale, ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa Rais wetu mpendwa Samia Suluhu Hassan ameshasaini mkopo wa trilioni 1.2 ambao unahusisha ujenzi wa barabara kadhaa, viwanja kadhaa pamoja na barabara ya kwenda Ruaha National Park inayopita Jimboni Kalenga.

Je, ni lini sasa Serikali tutegemee kuona kazi zinaanza kutekelezeka? Ahsante sana.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; napenda kujibu swali la nyongeza la Kiswaga, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, World Bank wameshakubali kuijenga barabara ya kutoka Iringa kwenye Ruaha National Park na ni kati ya hizo fedha ambazo ni 1.7 trillion. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo sasa kinachosubiriwa tu nikuanza taratibu za manunuzi. Ahsante.

MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa barabara ya Dareda - Dongobesh usanifu wa kina umeshakamilika; je, ni lini zabuni zitatangazwa ili ujenzi huu uanze mara moja?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara ya Dareda - Dongobesh imeshakamilika kwa kufanyiwa usanifu wa kina. Kwa hiyo, kwa sasa Serikali ipo kwenye hatua za kutafuta fedha ili barabara hiyo iweze kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na juhudi kubwa za Serikali ya Chama cha Mapinduzi kutujengea barabara ya mwendokasi kutoka Bendera Tatu mpaka Mbagala Rangitatu, lakini bado kuna changamoto kubwa katika maeneo ya Rangitatu.

Je, Serikali lini itakamilisha kujenga tena upya na vizuri kwa kiwango cha lami barabara kutoka Mbagala Kokoto - Rangitatu kwenda Kongowe - Mwandege? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dar es Salaam kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli barabara hii imekuwa na changamoto kubwa hasa ya foleni na Serikali sasa imeiweka kwenye mpango barabara hii ili iweze kujengwa upya na kupunguza foleni kubwa ambayo ni adha kubwa sana kwa wakazi wa Mbagala kwenda Kongowe, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa barabara inayopitiwa na Mlima Kitonga ni barabara ambayo imekuwa ikipata ajali nyingi na imekuwa ikipitisha mpaka wagonjwa wanaopelekwa hospitali ya Muhimbili.

Je, Serikali sasa iko tayari kujenga kwa kiwango cha lami barabara mbadala ili kama magari yakichelewa kupita pale kwa siku mbili au siku tatu; barabara ya Mahenge - Udekwa inayokwenda kutokezea Ilula ili wananchi waweze kupita kama magari yamekwamwa muda mrefu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Iringa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimjulishe Mheshimiwa Mbunge, kwanza kumpongeza kwa kutoa hilo wazo na sisi kama Serikali tumelichukua ili kweli kwamba kunapotokea changamoto basi tuwe na alternative ya kuweza kupitisha hasa kama kutatokea suala la wagonjwa kama alivyosema. Ahsante.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza katika Wizara hii ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya kutoka Kiranjeranje – Nanjilinji mpaka Ruangwa ni barabara ambayo imenadiwa katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2020 mpaka 2025, lakini pia imeshafanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina.

Je, lini Serikali itatenga fedha au kutenga bajeti kwa ajili ya kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi kwamba, azma ya Serikali ni kuzijenga barabara zote kwa kiwango cha lami na ndio maana tumeshaanza kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa tayari tumeshaanza hiyo ni hatua na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili tuweze kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri; sote tunatambua umuhimu wa eneo hili la Jangwani barabara ya Morogoro kama kiunganishi.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili (a) na (b); kwa sababu mvua zitaendelea kunyesha, tope, takataka, magugu, mafuriko yataendelea kuwepo na usumbufu upo kwa watumiaji wa pale.

Je, Serikali ina mpango gani wa dharura wakati tukisubiri huo mpango ambao utaratibu wake unaonekana kuchukua muda mrefu?

Swali la pili, hapo siku za nyuma Serikali ilitueleza mpango mzuri wa kuendeleza eneo lile la Jangwani ikiwemo kuunganisha na kupitia pembezoni mwa mto mpaka Salender Bridge pamoja na kuwekwa viwokwe. Naomba kuuliza Serikali mpango ule mzuri wa kuendeleza eneo lile la Jangwani umefikia wapi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tuna mpango wa dharura ambao unatumika kuhakikisha kwamba daraja lile linapitika na ndiyo maana utaona pamoja na kwamba mvua zinanyesha, lakini bado daraja linaendelea kupitika. Tumemuweka mkandarasi kwa lile daraja ambaye kila baada ya mvua kunyesha anaondoa mchanga, udongo na taka ngumu mita 500 juu na mita 500 chini ili kuruhusu maji yaweze kupita na changamoto hii inasababisha tu na watu kufnayakazi karibu na mto ule. Kwa hiyo, nitoe pia rai kwa wanaofanyakazi wasifanye kazi karibu na kingo za mto ambazo zinasababisha kushindwa kupitika kwa maji kwenye daraja.

Mheshimiwa Spika, suala la pili alilouliza mpango wa kuendeleza Bonde la Jangwani ni kweli upo kupitia mpango wa DMDP, lakini pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wabunge wa Dar es Salaam ambao walikaa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, TAMISEMI pamoja Hazina kwamba Serikali imeamua kwamba itajenga flyover ambayo itakuwa inaunganisha makutano ya fire na makutano ya Magomeni, ahsante.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Kutokana na mvua nyingi zilizonyesha mwaka jana kuna madaraja matatu ndani ya Wilaya ya Ludewa ambayo yapo chini ya TANROADS yaliharibika. Eneo la Muhoro, Nyapandi na Ludewa Vijijini, je, lini Serikali itajenga madaraja ya kudumu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mgaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nataka nimuhakikishie Mbunge kwamba baada ya changamoto ya hayo madaraja bahati nzuri mimi nimekwenda na nimefika na tumefanya ukarabati na tunachokifanya sasa hivi katika bajeti hii ni kuagiza madaraja mengi ya vyuma ambayo yatatumika pale panapotekea changamoto ili kuweza kuokoa na kufanya matengenezo ya haraka ili kurudisha mawasiliano, ahsante.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa eneo la makutano ya Mkwajuni, Kinondoni na Mto Msimbazi hukumbwa na mafuriko kipindi cha mvua kama ilivyo Jangwani na hivyo kusababisha adha kubwa sana kwa wananchi wa makazi hayo.

Mheshimiwa Spika, swali langu; je, Serikali ipo tayari kujenga daraja la kudumu ili kuondoa kero hii kwa wananchi ambayo imedumu kwa muda mrefu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lambert Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja alilotaja pia ni sehemu ya Bonde la Jangwani ambalo litafanywa pamoja kwenye Mpango wa DMDP ili kuboresha usafiri katika eneo hilo. Ahsante.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante; je, ni lini Serikali itajenga daraja linalounganisha Kalya na Ilagala katika Mto Malagarasi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja hili tunaita daraja la Malagarasi Chini na daraja hili pana kivuko kwa hiyo kuanzia mwaka huu wa fedha na mwaka unaokuja tunaendelea na tumetenga fedha ambapo tutakamilisha kufanya usanifu kwa ajili ya maandalizi ya kujenga daraja la kudumua kuunganisha Kigoma na eneo Kalya, ahsante.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; Daraja la Mto Mlokola ambalo lipo ndani ya Kata ya Mlokola ni daraja ambao lina hali mbaya sana na juzi tu limesababisha ajali kubwa iliyogharimu maisha ya wananchi wangu ndani ya Jimbo la Kwela.

Je, ni lini Serikali itatengeneza daraja hilo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante na napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deus Sangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimuagize Meneja wa TANROADS aende kwenye daraja hili akafanye tathmini ili tujue changamoto na tuone gharama ili tuweze kurejesha mawasiliano ya daraja hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amelitaja, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, barabara ya Mafinga kwende Mgololo eneo la Itulavano, daraja lililopo ni jembamba sana na barabara hii inatumika na malori yanayobeba mazao ya misitu.

Je, Serikali ipo tayari kulirekebisha na kulijenga daraja hili ili liwe pana kumudu magari hayo mazito? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii barabara aliyoitaja ndiyo barabara ambayo kwa asilimia kubwa inapitisha mbao sehemu kubwa ambazo tunaziona, lakini barabara aliyoitaja pamoja na daraja iko kwenye mpango wa kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami ikiwa ni pamoja na kulijenga hilo daraja ambalo litaendana na barabara hiyo, ahsante. (Makofi)
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Kwa kuwa ujenzi wa madaraja haya ya juu (flyovers) yamekuwa yana lengo la kupunguza foleni, lakini baada ya ujenzi wenyewe tu kunakuwa na kuwekwa matuta sasa kwenye barabara ambayo inakwenda ku-distort au kuharibu ile dhima ya kujenga zile flyover.

Je, ni ipi kauli ya Serikali juu ya mkanganyiko huu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli lengo la flyover ni kupunguza foleni na hili alilolisema wakati fulani inakuwa ni kwa ajili ya usalama kwamba tuweke matuta ili kupunguza ajali. Kwa hiyo, tutazingatia kuona kama hakuna ulazima wa kuweka hayo matuta tutayaondoa, lakini tukizingatia sana kwamba usalama wa wale watumiaji wa hizo barabara, ahsante.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga daraja linalounganisha kati ya Mbweni na Mapinga, Bagamoyo ili kupunguza foleni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Kibaha kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, daraja alilolitaja pia ni barabara ambayo ipo kwenye bajeti ya mwaka huu kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami na tunapojenga barabara hizo ni pamoja na madaraja yanayohusika kwenye hizo barabara, ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa tayari upembuzi yakinifu unaelekea mwisho na barabara hii kwakweli ni muhimu sana kwa wanachi wa Jimbo la Nyamagana hususani takribani kata tano za Mkuyuni, Mahina, Mhandu pamoja na Butimba; sasa Serikali ipo tayari kuhakikisha kwamba baada tu ya upembuzi yakinifu barabara hii inaanza kujengwa?

Mheshimiwa Spika, pili; barabra hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais; ni lini sasa Serikali itakuwa tayari kuhakikisha ahadi za Mheshimiwa Rais zinatimizwa kwa wakati? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ni kweli ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wakati huo akiwa ni Makamu wa Rais na sasa ni Rais na ndiyo maana barabara hii tayari tumeshaanza kutekeleza ahadi na tayari tunaifanyia usanifu ili iweze kukamilika na tuanze kuijenga kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, na barabara hii kwa swali lake la pili; tunaipa uzito mkubwa sana kwa sababu ni barabara ambayo tunaamini inakuwa ndiyo barabara kama bypass kwa mtu akitokea Nyegezi kwenda Mwanza Mjini ikitokea changamoto yoyote basi hii barabara ndiyo inayoweza kutumika kwa ajili ya kuwapeleka watu katikati ya Mji wa Mwanza. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa na mimi ningependa kujua je, ni lini Serikali itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami barabara ya Mbalizi - Mkwajuni - Makongorosi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja tayari ipo kwenye ukamilishwaji wa kufanyiwa usanifu wa kina na baada ya hapo Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami ili kuiunganisha Mkoa wa Mbeya kwa maana ya Wilaya ya Mbeya na Wilaya ya Songwe kwa Mkoa wa Songwe, ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa barabara kutoka Iringa kwenda Pawaga kupita Kihwele - Kalenga ipo kwenye kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Je, ni lini sasa Serikali itaweza kuijenga kwa kiwango cha lami? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara iliyotajwa ipo kwenye Ilani lakini tu nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hatuwezi tukaanza barabara zote kwa mwaka mmoja. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kadri tutakavyokuwa tunakwenda basi hii barabara itakuwa ni moja ya barabara ambazo zitajengwa kama zilivyoainishwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itajenga barabara ya Nangwa - Kisambara - Mkondoa ambayo vinaunganisha Mkoa wa Manyara na Kondoa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Samweli Hhyuma, Mbunge wa Hanang kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni kati ya barabara ambazo zipo kwenye mpango wa kuzijenga kwa kiwango cha lami, lakini ujenzi huo utategemea na upatikanaji wa fedha. Ahsante.

MHE. KILUMBE S. NG'ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii; ahadi ya Mheshimiwa Rais imetolewa pia katika Manispaa ya Kigoma Ujiji ya kujenga barabara ya kilometa 10. Ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa ahadi hiyo ya Rais?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ahadi za Rais zinapewa kipaumbele na Serikali inatafuta fedha ili kukamilisha ahadi hiyo kwa kujenga hizo kilometa 10 ambazo zimeahidiwa na Mheshimiwa Rais. Ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais ya kujenga barabara ya Mbuyu wa Mjerumani kupitia Magara hadi Mbulu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais ilitolewa wakati anazindua barabara ya Magara na tayari tumeshaanza kufanya usanifu kama alivyoagiza ikiwa ni maandalizi kuijenga barabara hiyo ya kutoka Mbuyu wa Mjerumani - Magara hadi Mbulu kwa kiwango cha lami.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, kutokana na ahadi ya Serikali barabara yetu ya Ubena Zomozi – Ngerengere je, lini itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Taletale Mbunge wa Morogoro Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara iliyotajwa imetengewa fedha katika bajeti hii kuianza kuijenga kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; Mji wa Bunda uliahidiwa kujengwa kilometa 10 barabara za mjini kwa kiwango cha lami ni lini sasa zitajengwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa kusaidiana na Wizara yangu pamoja na TAMISEMI tutahakikisha kwamba ahadi iliyoahidiwa inatimizwa na Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kujenga zile kilometa 10 katika Mji wa Bunda. Ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante na nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini naomba niweke kumbukumbu sawa, barabara hii ina urefu wa zaidi ya kilometa 25, lakini hizo kilometa 25 ndizo ahadi ziko kwenye Ilani ya CCM kwamba zitajengwa kwa kiwango cha lami na barabara hii ndiyo barabara pekee inayotoa wananchi wa Hagati kuja mjini ni barabara pekee hiyo hiyo tu.

Mheshimiwa Spika, swali langu nimeuliza ni lini Serikali itajenga kwa kiwango cha lami barabara hii?

Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili; barabara hii inaenda mpaka Nyasa, kwa hiyo, kule chini bado haijafunguliwa, je, Serikali iko tayari kuifungua barabara hii hadi kufika Wilaya ya Nyasa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante na napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, barabara hii tunatafuta fedha ili iweze kujengwa yote kwa kiwango cha lami, lakini Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami kwamba barabara hii inapita kwenye maeneo mengi yenye miinuko na makorofi na ndiyo maana Serikali iliona bora ianze kwanza kwa kujenga kwa kiwango cha lami yale maeneo yote ambayo ni korofi ili iendelee kupitika lakini maeneo mengine yakiwa ya changarawe.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kuifikisha hii barabara hadi Nyasa naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwakuwa tunaona ni barabara muhimu kuunganisha Mbinga na Nyasa, Wizara yangu kusaidiana na wenzetu wa TAMISEMI - TARURA tutakubaliana namna ya kuhakikisha kwamba tunafungua hii barabara hadi Nyasa ili kurahisisha mawasiliano kwa wananchi hawa. Ahsante.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya Simbo – Kalya kwa kiwango cha lami? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nashon Bidyanguze, Mbunge wa Kigoma Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya Simbo – Kalya ipo kwenye Ilani na Serikali inaendelea kutafuta fedha lakini kabla ya kuijenga barabara hii Serikali kwanza imeamua ijenge daraja la kudumu la Mto Malagarasi Chini na hatua ya pili itakayofuata itakuwa ni kutafuta fedha kuijenga barabara hiyo kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, mwaka 1973 Serikali ilifanya uamuzi wa kujenga Kiwanda cha Nguo cha Mbeya Textile cha pale Mbeya na lengo lilikuwa ni kwamba kiwanda hicho kitapata malighafi ya pamba kutoka katika Mikoa ya Shinyanga, Tabora na Mwanza kupitia barabara kutoka Tabora hadi Mbeya.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa sababu barabara hiyo haijajengwa hadi leo, kiwanda kile kilikufa. Je, Serikali itajenga lini hiyo barabara kutoka Tabora hadi Mbeya hususan kipande cha kutoka Ipole hadi Rungwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Ipole – Rungwa hadi Makongolosi ni barabara kuu na ni barabara ambayo ipo kwenye mpango na imetengewa fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, kuanza kwa barabara hii kutategemea tu na fedha itakavyopatikana, lakini tayari ipo kwenye mpango kwa ajili ya kuijenga barabara hii. Ahsante.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni tumeona kwenye vyombo vya habari, Serikali imekamilisha mazungumzo na Benki ya Dunia, hivyo kupelekea kupata fedha za ujenzi wa barabara kutoka Mtwara - Mingoyo hadi Masasi kilometa 201. Je, sasa ujenzi huo utaanza lini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chikota kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Rais katika jitihada za kufungua nchi na kuboresha usafirishaji, World Bank wako tayari kuijenga barabara ya Mingoyo hadi Masasi, barabara kuu ambayo ilikuwa kwa kweli imechakaa. Kuanza kwake kutategemea tu na jinsi taratibu za fedha kuhamisha kutoka World Bank kuja kwetu itakavyokuwa zimekamilika, barabara hii itaanza mara moja baada ya kupokea hizo fedha. Ahsante.

MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, barabara ya Rujewa – Madibila – Kinanyambo - Mafinga ni muhimu sana kwa wananchi wa Mbarali na upembuzi yakinifu ulishafanyika; je, ni lini sasa Serikali itaanza rasmi ujenzi wa barabara hii kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Francis, Mbunge wa Mbarali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hii ni barabara moja muhimu sana na ya kiuchumi na ni fupi kutoka Igawa – Rujewa kuja Mafinga. Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuijenga barabara hii kwa kiwango cha lami kwa ajili ya kuboresha usafiri kati ya Mbarali na Mafinga. Ahsante.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, barabara ya kutoka Masumbwe – Rugunga - Ushirika kwenda kuunganishwa na Mkoa wa Geita, lini itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maganga, Mbunge wa Mbogwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoiainisha itajengwa kadiri fedha zitakavyopatikana kwa kiwango cha lami, ahsante.

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi.

Mheshimiwa Naibu Waziri barabara ya kutoka Chala - Mpalamawe ilikuwa ni ahadi ya Rais wa Awamu ya Tano, pia ilikuwepo kwenye Ilani, lakini sasa hamuitamki. Nataka kujua, mna mpango gani wa kuijenga kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja ni barabara kuu, lakini ni barabara ambayo kwa sababu barabara nyingine ilikuwa inapita kwenye Makao Makuu ya Wilaya, Serikali iliamua kwanza ijenge barabara kupitia Makao Makuu na hii ifuate. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kadri Serikali itakavyopata fedha barabara hii pia itajengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naulizia barabara ya Kibiti kupitia Dimani kwenda Mloka kwenye Bwawa la Mkakati la Mwalimu Nyerere ni lini itajengwa kiwango cha lami? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoianisha inakwenda kwenye Bwawa la Nyerere na ni barabara ambazo Wizara inaangalia uwezekano kama alivyosema Mheshimiwa Waziri ziingie kwenye mpango wa EPC+F ili kuweza kuiharakisha kuijenga barabara hii, ahsante.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi ambayo imetajwa kufanyika lakini katika mvua za masika ambazo zimenyesha na kumalizika juzi hili eneo lilibomoka maji yakafurika na magari yakashindwa kupita.

Sasa swali langu liko hivi bila shaka huyu mkandarasi aliyefanya kazi hiyo alilipwa; je, Serikali ilijiridhisha kabla ya kumlipa mkandarasi kwa kazi aliyofanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; eneo hili ni eneo la Tingatinga na ni la miaka mingi, je, Serikali haioni haja kwamba panastahili kufanyika upembuzi yakinifu makini na kwa kutumia wataalamu makini ili eneo hili liweze kutengenezwa kwa ufanisi?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla ya kufanya malipo yoyote lazima Serikali ijiridhishe kwamba kazi iliyofanyika inahitaji malipo. Lakini nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kipindi cha mvua hata nyumba kama hii inaweza ikaondolewa na mvua. Kwa hiyo, suala la mvua ni suala lingine, lakini nachotaka kumwakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tathmini ilifanyika na kazi ilikuwa imefanyika lakini mvua inaponyesha haiwezi ikaondoa kitu chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili kwa kuwa tathmini ilifanyika na eneo tunalojenga tuta walishafanya tathmini. Kwa hiyo tuna uhakika kwamba tutaendelea kuliinua hilo tuta na ndio maana tunaongeza madaraja na kuinua tuta ili eneo hilo ambalo Mheshimiwa Mbunge anafahamu ni swamp area tuta lazima liinuliwe na ndio maana tumeongeza madaraja ili yaweze kupitisha maji yasiweze kukwama, ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Mbeya kwenda mpaka Dar es Salaam eneo la changarawe maarufu kama Jinja wakati wote limekuwa likisababisha ajali na kuuwa Watanzania walio wengi; na hivi majuzi Watanzania takribani 20 walifariki. Serikali ina mkakati gani kufanya tathmini hata ikibidi matengenezo kuhakikisha kwamba eneo lile haliendelei kuchukua roho za watu ambao hawana hatia?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kutoa pole kwa wananchi wengi ambao siku za karibuni tumesikia wamepoteza maisha katika eneo hilo la Majinja katika Wilaya ya Mufindi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na ukweli kwamba eneo hili limeendelea kusababisha ajali nyingi Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi imeshawaagiza makao makuu TANROADS pamoja na TANROADS Mkoa wa Iringa kuunda timu ambayo itakwenda kufanya study kujua tatizo ni nini ambalo limeendelea kusababisha ajali katika eneo hilo, ili kama ni suala la utaalamu kwa maana ya miundombinu ya barabara timu hiyo iweze kuishauri Serikali nini kifanyike ili kuondokana na ajali kama zinasababishwa na namna yoyote ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa hatua za haraka tumewaagiza TANROADS Mkoa wa Iringa waweze kuweka alama nyingi za kutoa tahadhari kwamba eneo hili ni hatari ikiwa ni kuona pia uwezekano kama wanaweza kuongeza matuta ili kupunguza ajali ikiwa hiyo ni hatua za muda mfupi, ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; barabara inayotoka Ntobo - Busangi mpaka Didia kwa muda mrefu imekuwa haina matengenezo. Sasa nilitaka kufahamu ni lini Serikali itaweza kuweka matengenezo ya kudumu kwenye barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara aliyoitaja imetengewa fedha kwa mwaka wa fedha unaokuja kwa ajili ya matengenezo ya barabara hiyo kwa mwaka huo unaokuja. Kwa hiyo, nina hakika katika mwaka unaokuja barabara hiyo itatengenezwa na tutahakikisha kwamba pengine yale maeneo yote ambayo hayapitiki ndio yanayopewa kipaumbele katika matengenezo hayo. Ahsante.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona; Serikali ilianzisha mchakato wa kujenga daraja jipya la Kikafu, na tayari kwa muda mrefu sana ilifanya tathmini kwa wananchi kupisha maeneo yao ili daraja hilo liweze kujengwa.

Swali langu ni lini Serikali italipa fidia wananchi wale waliofanyiwa tathmini na kuanza ujenzi wa daraja la kikafu?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ambayo anaitaja daraja liko kwenye barabara kuu ya Arusha - Moshi kwenda Holili, na daraja hili lipo kwenye mpango katika bajeti ambayo tumeshaipitisha. Kabla ya kuanza ujenzi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kipaumbele kitakuwa ni kwanza kuwalipa wananchi ambao wanapisha daraja hili kwa sababu tunalihamisha kabisa lilipokuwa na kulipeleka sehemu nyingine, ahsante.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona, barabara ya kutoka Dar es Salaam hadi Mbeya eneo la Mlima Kitonga limekuwa na ajali nyingi na mara nyingi kuziba barabara hiyo na kusimamisha shughuli za kiuchumi kwenye nchi yetu. (Makofi)

Ni lini sasa Serikali itafanya utaratibu au kuipanua barabara ile au kuangalia njia mbadala ili shughuli za kiuchumi zisisimame wakati kunapotokea ajali kwenye eneo lile?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justin Nyamoga, Mbunge wa Kilolo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli eneo la Kitonga ni eneo lenye barabara ambayo ina miinuko na kona kali na Serikali imeendelea kulifanyia matengenezo ikiwa ni pamoja na kujenga zege, kuondoa kona na kuipanua ile barabara ili kuhakikisha kwamba magari mengi na hasa ambayo ni malori yanapishana kwa urahisi.

Suala lingine ambalo sasa tunafikiria ni kuimarisha barabara ambayo ni ya bypass ili kunapotokea changamoto na barabara ikiziba basi magari hayo yaweze kupita njia ya bypass, ahsante.
MHE. DKT. FAUSTINE E. NDUNGULILE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; nataka kujua kwamba kwa sasa kimebaki kiasi gani cha deni la gharama za ujenzi ambacho kimebaki?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; kwa mujibu wa majibu ambayo amenipa kwamba tarehe 21 Mei, 2022 walifanya mapitio ya tozo za daraja na kuanzisha utaratibu wa tozo za siku, wiki na mwezi. Je, ni lini utaratibu huu wa tozo za siku, wiki na mwezi utaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Faustine Ndugulile, Mbunge wa Kigamboni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inakamilisha mfumo wa kuanza tozo kwa siku, wiki na mwezi; nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunategemea kwamba kuanzia tarehe 1 Julai, 2022, mfumo huu utaanza kutumika. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Swali la kwanza; kwa kuwa Serikali imeshakamilisha upembuzi yakinifu na usanifu wa kina kwa kipande cha kutoka Solwa kwenda Salawe kilomita 15, je, ni lini ujenzi utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa sehemu ya Solwa – Iselamagazi yenye kilomita 64.66, upembuzi unaendelea. Je, ni lini huo upembuzi utakamilika ili ujenzi uanze? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa utaratibu uliopo ni kwamba, kwa kuwa barabara hii ni moja itakuwa na lot moja kwa hiyo tunataka tupate tathmini ya gharama ya barabara nzima ili tuweze kupata gharama ya barabara nzima na kuianza kuijenga kwa kiwango cha lami kwa jinsi itakavyokwenda. Kwa barabara hii ambayo imebaki kilomita 64.66 kama tulivyosema, usanifu na upembuzi yakinifu unaendelea, tunategemea utakwenda kadri ya mkataba ulivyopanga na tunaamini kwamba kabla ya mwisho wa mwaka huu 2022, usanifu utakuwa umekamilika. Ahsante.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; barabara hii iliyofanyiwa tathmini, je, ni lini wananchi wake watalipwa fidia zao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; miezi miwili iliyopita, nilihudhuria utiaji saini Mkataba wa BRT, awamu ya tatu ambao umejumuisha ujenzi wa kipande kilichobakia cha Barabara kutoka Tamko kuja Mapinga Bagamoyo. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kipande hiki cha barabara?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli Barabara hii ya Makofia - Mlandizi tulishakamisha usanifu na tulifanya tathmini kwa maana kupata gharama ya fidia mwaka 2018, lakini hatukufika mpaka mwisho. Kwa hiyo zoezi hilo limerudiwa na Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi kwamba tayari watu wameshapita na hatua ambayo tunayo sasa hivi, ni kupata uhakiki ili jedwali la malipo liende Hazina kwa ajili ya kuandaa malipo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, zoezi hilo linaendelea na watalipwa baada ya kuhakikiwa na kuridhika kwamba hiki ndio kiasi ambacho wanatakiwa walipwe hao ambao wataipisha hiyo barabara.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala lake la pili ni kweli Barabara ya Tamko – Mapinga tulishatia saini na nakiri kushiriki. Mheshimiwa Mbunge, atakubaliana nami kwamba, barabara hii haikuwa na hifadhi ya kama barabara. Sasa Mkandarasi kuna mambo ya kimkataba ambayo anakamilisha na sisi kama Serikali tuko tunamfuatilia kuona anakamilisha zile taratibu ili aanze kuijenga na tuko kwenye hatua za mwisho, barabara hiyo sasa itaanza kujengwa kwa sababu tayari tulishawekeana saini, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Barabara ya kutoka Tarime Mjini mpaka Mugumu ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Tanzania na Mkoa wa Mara kwa ujumla kwa sababu inaunganisha kwenda kwenye utalii na ilitengewa fedha kuanzia mwaka 2021/2022, takribani bilioni 35, lakini Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa kusuasua mpaka sasa hivi imepeleka bilioni tano tu.

Je, ni lini, Serikali itahakikisha kwamba inampelekea mkandarasi fedha kwa wakati ili aweze kukamilisha ile barabara kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge Matiko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara hii ni muhimu na hii barabara imegawanywa katika lot mbili, hatupeleki hela yote, tunalipa kulingana na mahitaji ya mkandarasi. Kwa hiyo akishaleta hati ya malipo ndipo tunapomlipa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali itaendelea kulipa kadri hati zinavyokuja kuhakikisha kwamba barabara yote ya Tarime - Mugumu inakamilika, ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kilometa 54 za lami kwa wananchi wa Ushetu ambapo Serikali iliahidi yenyewe, lakini hakuna dalili yoyote inayoendelea?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni kweli kwamba Serikali iliahidi kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami. Barabara zote zinazofanana na hiyo ya Ushetu, mpango wa Serikali ni kuzijenga kwa kiwango cha lami, lakini utakubaliana nami kwamba hapa ndio tunapopitisha bajeti, kwa hiyo bajeti ndio inayoamua. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi tutaendelea kuweka kwenye mipango ile ahadi ya Serikali ambayo tuliahidi iweze kutimia kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Barabara ya Mgololo - Mafinga itajengwa kwa kiwango cha lami kwa sababu hii barabara ni kitega uchumi katika Jimbo la Mufindi Kusini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara ya Mgololo – Mafinga ni kati ya barabara sita ama saba ambazo tunazijenga kwa utaratibu wa EPC + F na nimelijibu mara kadhaa kwamba tayari kazi zinaendelea za awali kwa wakandarasi ambao wamepatikana kuijenga hii barabara. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hii ni kati ya barabara ambazo zinatekelezwa kwa Mpango wa EPC + F na tutahakikisha kwamba hiyo barabara inajengwa kama Serikali ilivyoahidi, ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa, barabara ya Utegi – Shirati mpaka Kihongwe Upembuzi yakinifu na usanifu wa kina umekwishakamilika na barabara hii tayari imetengewa fedha. Ninataka kujua kwa Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa barabara hii itatangazwa na kuanza ujenzi wa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chege, swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli bahati nzuri barabara hii nimetembelea tukiwa na Mheshimiwa Mbunge na aliahidiwa kwamba barabara hii itaanza kujengwa. Barabara hii ipo kwenye mpango wa kuanza kuijenga kwa kipindi cha bajeti hii ya 2023/2024. Kwa hiyo, taratibu za kuandaa tender document zinaendelea, basi zikikamilika barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi. Ujenzi wa barabara ya kutoka Kabingo hadi Kibaoni kilometa 25 kwa kiwango cha lami unasuasua sana.

Je, ni lini Serikali itakwamua ujenzi wa barabara hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii inayoisema ni Kibondo link, barabara ambayo inajengwa kwa kiwango cha lami. Nimeitembelea hiyo barabara kuangalia changamoto zilizopo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeshaona changamoto zilizokuwepo za kiutendaji kwa Mkandarasi na tuna hakika baada ya kukaa nae barabara hii sasa itaanza kwenda kasi ili tukamilishe zile kilometa 25. Ahsante.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara ya MR – Pawaga kwa kiwango cha lami kuanzia MR – Iringa Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi kwamba katika bajeti ya mwaka huu kuna kiasi kimetengwa kwa ajili ya kuanza kilomita kama sikosei ni kilometa kama 20 kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, kadri tutakavyokwenda taratibu zikishakamilika barabara hizo zitatangazwa kwa ajili ya kuanza kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ningependa kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri; barabara ya Nkome – Nzela – Geita yenye urefu wa kilometa 20 mwaka wa tatu Mkandarasi amepatikana tunasubiri kusaini.

Je, huna mafuta nikuwekee ili tuende tukasaini kesho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan haiwezi kukosa mafuta ya kwenda kusaini, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tunatambua umuhimu wa hiyo barabara ni suala la muda tu na ipo kwenye mipango, muda ukifika nina hakika barabara hii tutaisaini kwa sababu tayari imeishatengewa fedha na kila kitu kimekamilika. Kwa hiyo, tunachosubiri tu ni suala la taratibu zikamilike ili Mkandarasi aweze kuanza kazi hiyo ya kujenga kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, ahsante, Lindi na Mtwara tunashukuru kwa jitihada za Dkt. Samia Suluhu Hassan kutuletea maendeleo na ndiyo maana akaridhia kusaini kwa Mkataba huo wa EPC + F hapo Juni mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, kusaini mkataba ni jambo moja na kuanza ujenzi ni jambo lingine; je, ni lini sasa Mkandarasi ataanza kazi ya Ujenzi Masasi – Nachingwea – Liwale? (Makofi)

Swali la pili; je, ni lini sasa barabara ya Nachingwea kwenda Kilimarondo itajengwa kwa kiwango cha lami? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tecla Ungele, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Masasi – Nachingwea hadi Liwale kilometa 175 kama nilivyosema katika jibu la msingi inatekelezwa kwa utaratibu wa EPC + F na iko kwenye hatua kama ambavyo barabara zote zipo.
Mheshimiwa Spika, sasa hivi Waziri alitolea maelezo wako wanapitia usanifu wale Wakandarasi ambao wamepewa hizo barabara na tunategemea Januari wakandarasi watakuwa wako site baada ya kukamilisha zile taratibu zao za kupitia ule usanifu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hilo linaendelea na barabara hizo zitaanza kujengwa. Kinachoendelea tu hapa ni kwamba ni utaratibu ambao ni mpya kwetu sisi lakini wanatakiwa wale ambao wamepewa hizo kazi nao lazima wapitie usanifu na wajiridhishe.

Mheshimiwa Spika, swali la pili kuhusu barabara aliyoitaja hiyo kwenda Kilimarondo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara hiyo baada ya kufanyiwa usanifu bajeti ikiruhusu basi tutaanza kuijenga kwa kiwango cha lami, kwa sababu lengo la Serikali ni kuzijenga barabara hizi kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nami niulize swali moja la nyongeza.

Barabara ya kutoka Mtama – Kitangali hadi Amkeni – Newala, yenye urefu wa kilometa 74 ipo kwenye zoezi la Upembuzi Yakinifu, ni lini zoezi hili litakamilika ili barabara hii ijengwe kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, suala la upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ni suala ambalo linategemeana na aina ya barabara yenyewe. Kwa hiyo, mandhari tumeanza tunategemea kwamba, usanifu kwa urefu wa kilometa hizi 74 haziwezi kuzidi mwaka lakini namshawishi Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunategemea ndani ya mwaka mmoja baada ya kuanza usanifu utakuwa umekamilika wa hii barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Kwa kuwa ujenzi wa barabara ya Ifakara – Kidatu unakaribia kukamilika na kwa kuwa kumekuwa na ajali nyingi sana katika eneo la Mang’ula Kona kutokana na eneo la hifadhi kuingia barabarani, na kwa kuwa, kupitia Waziri wa Maliasili, Mheshimiwa Rais aliliridhia akatupatia eneo la hifadhi ili tuweze kupasafisha kusaidia magari kuonana, na kwa kuwa Waziri wa Ujenzialifika katika eneo husika akaahisi kwamba eneo hilo litasafishwa.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni lini ahadi hiyo ya kusafisha Mang’ula Kona itaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara anayoitaja hii ya Kidatu kwenda Ifakara ni barabara kuu na bahati nzuri kwenye hiyo kona ya Mang’ula Kona mimi nimefika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tayari Wizara ilishaelekeza baada ya maombi ya Mheshimiwa Mbunge lakini pia na Waziri kutoa maelekezo kwa Meneja wa Mkoa wa Morogoro aende akaangalie namna ambavyo watafanya kupunguza ile kona. Kwa sababu kupunguzwa kwa hiyo kona haikuwa sehemu ya usanifu wa hiyo Barabara, kwa hiyo lazima waende wakafanye usanifu mpya wa eneo na kuona gharama ya kufanya hiyo kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. AMANDUS J. CHINGUILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara ya Nanganga – Nachingwea kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, katika jibu la msingi nilisema kwamba barabara ya Nachingwea – Nanganga ipo katika hatua za mwisho na tunategemea katika zile barabara ambazo tunategemea kuzisainia kwa pamoja hiyo barabara ni mojawapo ya Nanganga – Nachingwea. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; nini mkakati wa Serikali sasa kujenga kwa kiwango cha lami Barabara ya Mtwara – Pachani na Nalasi – Tunduru ambayo upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ulishafanyika na ipo kwenye Ilani, na ndiyo tunayoisubiri barabara hii inayotegemewa na vijiji vingi zaidi ya 50 katika eneo hilo la Namtumbo na Tunduru? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunatambua umuhimu wa hii barabara ya Mtwara – Pachani hadi Nalasi – Tunduru ambayo ina urefu wa kilometa 300. Wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami, tulichoshauri na tunachokifanya sasa hivi katika barabara hiyo ni kwanza kuhimarisha madaraja ambayo ina madaraja mengi ya mito.

Pili, ni kujenga kwa kiwango cha zege ama lami maeneo yote ambayo huwa yanakwamisha usafiri katika hiyo barabara ili wananchi waendelee kupita kipindi chote wakati Serikali inatafuta fedha ya kuijenga barabara yote kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Ni takribani miezi mitano imepita sasa hivi tangu mikataba ya ujenzi wa barabara ya Mnivata – Nanyamba – Newala hadi Masasi imesainiwa.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, kwanza mimi niseme kama kuna barabara ambayo wenzetu hawatakiwi kuwa na wasiwasi ni hiyo barabara ya Mnivata – Newala kwenda Masasi.

Mheshimiwa Spika, taratibu ambazo zinaendelea sasa hivi ni taratibu za maandalizi kwa maana ya mobilization na wenzetu wa Benki ya Maendeleo ya Afrika ndiyo ambao tunasaidiana nao kuijenga hiyo hiyo barabara.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ni taratibu tu zinaendelea za kimkataba lakini muda siyo mrefu watawaona sasa wakiwa wako site katika hivyo vipande viwili, ambavyo barabara hiyo imegawanywa katika vipande viwili, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua au kurekebisha barabara ya Kilwa kipande cha Mbagala Zakheim kutoka Zakheim mpaka Mzinga, kwa sababu kipande hicho kimekuwa na changamoto, unatoka huko lakini unafika pale magari hayaendi, kunakuwa na msongamano mkubwa sana.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Spika, barabara zote za Dar es Salaam kulingana na ukuaji wa mji zinafanyiwa study kuona barabara zote ambazo zina changamoto zinafanyiwa marekebisho, ikiwa ni pamoja na kuongeza upana wa barabara hizo, na siyo za Dar es Salaam tu hata barabara za Mikoani ambazo zilijengwa zamani nyingi zilikuwa na upana mdogo.

Kwa hiyo, sasa hivi hizo barabara zinapitiwa upya ikiwa ni pamoja na barabara aliyoitaja ili kuhakikisha kwamba sasa tunakwenda kwa kipindi cha sasa kuzipanua hizo barabara, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa wananchi wa Haydom wameshawapa eneo la kujenga majengo ya mkandarasi ili aanze kazi na wewe ulikuja kusaini ule mkataba.

Je, ni lini anakuja kujenga yale majengo ili barabara ianze kujengwa ya Haydom – Labay?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, bahati nzuri hiyo barabara mkandarasi ambaye anajenga kipande cha kwanza ndiyo atakaejenga kipande cha pili. Kazi anayofanya sasa hivi ni kufanya usanifu, kwa sababu barabara hiyo inayojengwa ni sanifu inajengwa na atakapokuwa amekamilisha nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge ndipo atakapoanza sasa kujenga hiyo kambi yake eneo ambalo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Mbulu kwa kulitoa hilo eneo la ujenzi bure kabisa, ahsante. (Makofi)
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Je, ni lini Serikali sasa mtaanza ujenzi wa barabara muhimu ya kutoka Lujewa – Madibila mpaka Mafinga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Bahati Ndingo, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli hiyo barabara ni muhimu na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Mheshimiwa Rais akiwa ziara katika Mkoa wa Iringa alitoa maelekezo hiyo barabara ianze kujengwa kwa kiwango cha lami kilomita 25. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, sasa hivi tuko kwenye hatua za manunuzi kutekeleza hiyo ahadi na maelekezo ya Mheshimiwa Rais, ahsante. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua tunao ujenzi wa kilomita moja ya lami Mji wa Karumwa, takribani miezi 24 na tuta lile limenyanyuliwa zaidi ya mita moja, mvua zinaendelea kunyesha na maji yanaingia kwenye nyumba za watu imekuwa ni kero kubwa. Miezi 24 kilomita moja haijakamilika, nataka kauli ya Serikali ni lini kilomita moja hiyo itakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ninakiri kwamba, Mheshimiwa Mbunge amekuja ofisini kufuatilia hili suala, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mji wa Karumwa, nimeongea na Meneja wa Mkoa wa Geita kwamba hiyo barabara itakamilishwa. Sasa hivi kilichokwamisha tu ni kwamba mvua inanyesha na baada ya hapo kwa sababu ipo chini ya Meneja wa Mkoa wa Geita, wataikamilisha hiyo barabara ikiwa ni pamoja na kutengeneza hiyo mifereji ambayo inaleta adha kwa wananchi wa Karumwa, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwanza niseme tu nasikitika na majibu kwa sababu nilielekeza swali langu TANROADS kwa maana ya highways, lakini hapo anajibu vikundi vilivyosajiliwa na Halmashauri, Manispaa na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutumia teknolojia ya kisasa kwa maana ya magari yangeweza kuwa yanasafisha hizi highway usiku ambapo kuna msongamono mdogo sana wa magari. Nataka kujua, Serikali imeshafanya cost benefit analysis kuweza kujua matumizi ya vifaa vya kisasa vis a vis wanavyosafisha kwa mikono ina faida gani kwenye uchumi wa Kitaifa? Kwa maana vifaa vya kisasa vinapunguza msongamano wa magari, ajali na madhara mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali imeshafanya tafiti kuweza kujua madhara wanayopata wananchi wanaofanya usafi kwa mikono kusafisha barabara na mitaro? Wameshafanya tafiti za kiafya kujua madhara wanayopata wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, wazo la Mheshimiwa Mbunge Serikali imelichukua, hilo la kwanza.

Suala la pili, ni kwamba TANROADS pia ina barabara ambazo ziko katika Majiji, Miji, Manispaa na hata katika Halmashauri za Wilaya. Hayo maeneo ndiyo hasa ambayo yameonekana yanakuwa na uchafu mwingi ambayo yanahitaji kufanyiwa usafi. Hata hivyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi ya kufanya usafi wa barabara huwa tunatoa kwa wakandarasi na hawajalazimishwa kwamba ni lazima watumie watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana kwa sasa pale Dar es Salaam tayari tuna wakandarasi wawili ambao wameshaanza kutumia teknolojia hii ya kutumia magari kusafisha barabara zetu. Pia, namkumbusha Mheshimiwa Mbunge kwamba tuna Sheria inayotutaka katika kila mwaka vikundi vingapi, watu wangapi ambao wamepewa kazi hizi za kufanya usafi, kwa hiyo ni takwa pia la kisheria ambalo ni lazima tulitimize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema tutakapokuwa tumejiridhisha, kwamba kuna haja sasa pengine ya kubadilisha sheria kwamba tuelekeze zaidi kwenye matumizi ya vifaa vya kisasa, hilo litafanyika na ndiyo maana tumesema wazo hilo tumelichukua. Hili ni pamoja na kuangalia kama kuna madhara kiasi gani ambayo wanaofanya usafi kwa njia ya mikono ambavyo ni vikundi vya watu maalum hasa vikundi vya akinamama na vijana ambavyo mara nyingi ndiyo vitakuwa vinafanya kazi. Tutafanya hizo tafiti kwa kuwa hilo wazo tumelichukua na tutalifanyia kazi, ahsante.
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa fidia aliyoitaja Mheshimiwa Naibu Waziri ililipwa mwaka 2014 wakati barabara ilikuwa na upana wa mita 22. Mwaka 2017 walipokamilisha ujenzi wa barabara ile waliongeza mita nane kufika 30 na yenyewe ikachukua madarasa na nyumba ya malimu, na kwa kuwa Mheshimiwa Waziri Mbarawa alifika akaiona ile hali na akatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kutoa michoro pamoja na gharama na Mkurugenzi akafanya hivyo.
Napenda kujua sasa ni lini Serikali itatekeleza kupitia TANROADS ujenzi wa ile Shule ya Msingi Unkuku kwa sababu imeliwa sana na barabara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari niambatane naye pamoja na wataalam wake tukaione hii Shule ya Msingi Unkuku ilivyo katika mazingira hatarishi kwa watoto?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja. Ni kweli kwamba Serikali ililipa fidia wakati huo barabara ikiwa na upana wa mita 22.5. Kama alivyosema kwa sababu mimi mwenyewe sijaenda, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Kondoa na Dodoma ni karibu, nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaongozana, tutafute siku mimi pamoja na wataalam ili twende eneo la shule tukaangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, umetolewa mwongozo kwamba pale ambapo miundombinu ya shule, zahanati ama hospitali zinakuwa zimepitiwa na barabara kwa maana ya kuifuata, hatutakuwa tunatoa fidia badala yake tutakuwa tunajenga ile miundombinu yote iliyoathirika. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutakwenda na haya yote yatajibiwa ikiwa ni pamoja na kuona uwezekano kama kuna haja ya Serikali kujenga hiyo shule upya ama kutoa fidia, basi tutafanya hivyo baada ya kufika site, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili. Swali la kwanza; je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuweka fedha kwenye bajeti ijayo ili Barabara hii ya Ugalla - Kahama ikawa kwenye bajeti kwa uhakika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Barabara ya Dareda - Dongobesh aliiweka kwenye mpango wa kujengwa kwa kilomita tisa na mpaka leo haijaanza kujengwa. Je, ni lini ujenzi wa barabara hiyo utaanza?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara niliyoitaja kuna baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa hayajafunguliwa, kwa hiyo kitu cha kwanza ni kuifungua yote na kuikamilisha. Pia tuliona kwanza tufanye usanifu uliokamilika kwenye Daraja kubwa la Mto Ugalla, lakini kabla ya kufika kwenye Daraja la Mto Ugalla kuna madaraja madogo sita ambayo tumeanza kuyajenga ili kulifikia hilo daraja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutakapokamilisha ujenzi wa hayo ma-culvert, hatua ya pili itakuwa ni kujenga hilo daraja ili kuifungua barabara yote ambayo inaunganisha Mkoa wa Katavi – Tabora na Mkoa wa Shinyanga kwa upande wa Kahama. Kwa hiyo, tutakapokuwa tumekamilisha hii kazi sasa Serikali itaweka kwenye bajeti kuijenga barabara yote, lakini cha muhimu kwanza ni kukamilisha hayo madaraja ili kwanza tuifungue hiyo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali lake la pili la Barabara ya Dareda – Dongobesh, ni kweli tulikuwa tumepata mkandarasi, lakini ikatokea tatizo la kimkataba ambalo sasa limeshatatuliwa na tunategemea kukamilisha manunuzi ya hiyo barabara. Baada ya hapo naamini barabara hiyo inaenda kujengwa kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya jumla ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; ipo barabara ya Makabe – Msakuzi kuelekea Mpiji Magoe ambayo ina sifa hizo ambazo amezizungumza na sasa barabara hii imeanza kutengenezwa, wananchi bado wako kwenye sintofahamu kama watalipwa fidia au lah! Je, ni ipi kauli ya Serikali kwenye barabara hii. (Makofi)

Swali la pili, ipo barabara ya Victoria au inaitwa Mbezi Shule – Mpiji Magohe, kilometa 9.5; ni barabara ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais lakini ipo ndani ya bajeti kwa kipindi cha miaka miwili, lakini ina watu takribani 50,000 ambao ni wengi zaidi hata ya majimbo mengine.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge wa Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Makabe – Msakuzi, ni barabara ambayo tangu kuwepo kwake iko chini ya TANROADS na wakati ule ilikuwa chini ya ujenzi Mkoa wa Dar es Salaam, TANROADS ilipoanzishwa ikawa imehamia moja kwa moja TANROADS. Kwa hiyo, kwa wananchi ambao watakuwa ndani ya mita 22.5 kutoka katikati hawatastahili kulipwa, ila pale ambapo tutakwenda 7.5 wananchi ambao wako katika barabara hii watalipwa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu barabara ya Victoria, pale kuna barabara mbili, kuna barabara ya Kibamba Shule – Magoe Mpiji na Victoria kwenda Magoe Mpiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kibamba Shule tayari imeshaanza kujengwa kwa awamu, pia, ndiyo tunayoitegemea itakuwa outer ring road ya Mkoa wa Dar es Salaam na usanifu unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Victoria imekuwa ni barabara ambayo inahitajika sana hasa baada ya kuanzisha stendi ya Magufuli, tunavyoongea sasa hivi Mhandisi Mshauri yuko field kufanya usanifu na tunategemea baada ya kukamilisha kwa bajeti ambayo tunaiandaa iweze kuingia ili ijengwe kwa kiwango cha lami, ahsante. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza kabisa sijaridhika sana na haya majibu, lakini kwa kuwa Mheshimiwa Waziri anasema kwamba mzabuni tayari ameshapatikana…

SPIKA: Mheshimiwa ngoja, hujaridhika kwamba ni majibu hayana..., yaani siyo ya kweli, hayana uhalisia ama? Kwa sababu kanuni zetu zinataka swali lijibiwe kikamilifu. Hujaridhika kwa namna gani?

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, majibu haya hayana uhalisia.

SPIKA: Fafanua.

MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, naomba nifafanue. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri amesema kwamba mzabuni tayari amepatikana na anaenda kupata Msanifu Mshauri na kuianza kazi hiyo mwaka 2024 na kumaliza 2025. Kwa nini nasema kwamba halipo sawasawa, fedha ambayo ilikuwa imetengwa kwa ajili ya usanifu kwa mwaka wa fedha 2021 na kutolewa mwaka 2022, fedha hiyo ilitengwa shilingi milioni 300 na kutolewa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kuanza kazi hiyo mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, leo ananiambia anaenda kupatikana Msanifu mwaka 2024 na kumaliza kazi hiyo mwaka 2025, hapa majibu haya yanakinzana.

Mheshimiwa Spika, niendelee?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hata katika jibu langu la msingi, siyo kwamba Mhandisi Mshauri amepatikana. Ila tayari zabuni ya manunuzi kumpata huyo Mhandisi Mshauri, ndiyo tunakwenda kutangaza.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti ya 2022/2023 tulitenga bajeti kwa ajili ya kuanza kazi hiyo. Hiyo bajeti ambayo imetupelekea sisi kuanza kutangaza na hata katika mwaka huu wa fedha pia kwenye vitabu vyetu vya bajeti, bado tumetenga katika kuendelea kufanya hiyo kazi ya usanifu wa kina wa barabara hiyo, ahsante.

SPIKA: Sawa, hapo kwenye jibu lako panaposema hivyo, kazi zitakamilika mwezi Februari, 2025. Ni kazi zipi, hizi za usanifu ama za ujenzi?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, ni kazi za usanifu, kwa barabara ilivyo haiwezi ikafanyika…
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa sasa barabara hii ya Mbulu – Garbabi ni kweli Mkandarasi yupo site, lakini ana tatizo hilo la kutolipwa fedha baada ya yeye ku-raise certificate ambayo iko ofisini kwa Mheshimiwa Waziri. Je, lini atalipwa hiyo fedha ili aendelee kuweka au kumalizia barabara hii ya Garbabi kwenda Mbulu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nashukuru kwanza Mheshimiwa Naibu Waziri alikuwepo katika kusaini Mkataba wa Barabara ya kutoka Haydom kuja Labay. Sasa ni miezi sita, tumesaini tarehe 25 Mei, 2023. Je, ni lini sasa barabara hii itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami ili wananchi waweze kupita? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkandarasi ambaye anafanya kazi kati ya Mbulu na Garbabi, nataka kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba anaendelea na kazi kwa sasa. Hii ni baada ya Mkataba wake unamtaka asisimame kazi baada ya kuanza kazi. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, nimepata taarifa leo kwamba kazi zinaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipande alichokisema cha Labay – Haydom, ni kweli kilisainiwa. Nataka kumkumbusha Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu unaotumika katika kipande hiki ni sanifu na jenga. Wajibu wa Mkandarasi kwanza ni kufanya usanifu wa ile Barabara. Halafu ikishasanifiwa ipate kibali kwamba iko sawasawa na Mamlaka kwa maana ya TANROADS ndipo anatakiwa sasa aanze kujenga hiyo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hizo zinaendelea na akishakamilisha, basi tutamwona site akiwa anaanza kuijenga hiyo barabara, ahsante. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Barabara ya Moshi – Arusha hasa kipande cha pale Moshi Mjini itapanuliwa ukilinganisha kwamba tayari Mikataba ilishasainiwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kweli kwamba barabara hii inapanuliwa kutoka Arusha kwenda Moshi ikiwa ni pamoja ya lile Daraja la Kikafu. Hii barabara ambayo ameisema, tunasaidiana na wenzetu wa JICA. Ziko taratibu ambazo zikishakamilika, basi barabara hii itaanza kujengwa, lakini iko mbioni kuanza kujengwa. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Barabara ya Omurushaka kwenda mpaka Mrongo, Mkandarasi amepatikana ni zaidi ya miezi sita lakini bado Mkataba haujasainiwa. Je, ni lini Mkataba utasainiwa ili barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Moja ya swali ambalo alitolea ufafanuzi Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi, ni kwamba Barabara aliyoitaja Omurushaka kwenda Murongo, kilometa 50 ni kati ya zile barabara kuu 15 ambazo tayari tumeshaomba kama alivyosema Mheshimiwa Waziri zisainiwe zote kwa pamoja ambazo zinagharimu karibu shilingi Trilioni 2.0. Alishasema kwamba aliomba Mamlaka ziweze kusimamia hilo zoezi, kushuhudia. Kwa hiyo namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba barabara hiyo ni kati ya barabara hizo ambazo zitapata kibali cha kuanza kuzijenga, ahsante. (Makofi)
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwa kuwa Mwezi Juni mwaka huu tulisaini Mkataba wa Barabara ya Karatu – Mbulu – Haydom – Lalago. Je, ni lini kazi rasmi itaanza ya ujenzi wa kipande cha Karatu – Mbulu ambako kipindi hiki cha mvua wananchi wanapata matatizo makubwa?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipande cha Karatu – Mbulu ni kipande ambacho kinaangukia kwenye zile barabara ambazo zinajengwa kwa Mpango wa EPC+F. Tayari Wakandarasi washasaini, wako site wakiwa pia wanafanya, tunasema usanifu wa kina kwa sababu usanifu waliopewa ni wa awali. Baada ya kukamilisha taratibu zote kama tulivyosema, barabara hizi zitaanza kujengwa kuanzia Januari, ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha Barabara inayoanzia Njuki – Ilongero – Haydom kwa kiwango cha lami hasa ukizingatia ujenzi wake umekuwa ukisuasua. Barabara hii ina ahadi ya viongozi toka Awamu ya Nne? Napenda kupata commitment ya Serikali, ni lini barabara hii itakamilika kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kama alivyosema ahadi za viongozi, namhakikisha Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara hizi zote ambazo zimepangiwa bajeti kwa mwaka huu, yako maandalizi ambayo yanaendelea kuhakikisha kwamba tunaanza ujenzi kama tulivyopanga kwenye Bajeti ya mwaka huu 2023/2024, ahsante.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga Barabara ya kutoka Kalela – Munzeze – Buhigwe kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Genzabuke kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii ni barabara ya mkoa ambayo namkumbusha Mheshimiwa Mbunge kwamba ilikuwa haijafanyiwa usanifu. Sasa hivi barabara hiyo inakamilishwa kufanya usanifu kutoka Kalela – Munzeze – Buhigwe. Baada ya hapo gharama zitajulikana, Serikali sasa itatafuta fedha kwa ajili ya kuijenga kwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Kwanza natumia nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia Serikali anayoiongoza ya Awamu ya Sita kwa kuwa msikivu sana kwa kilio cha wajasiriamali, Wilaya ya Ubungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo maswali mawili ya nyongeza, swali la kwanza; kwa kuwa ni kawaida sana vinavyotengenezwa vibanda hivi vya wajasiriamali, wananchi mbalimbali kutokea kwenye maeneo mbalimbali ya nchi wanavamia na kusababisha walengwa kutofikiwa.

Je, Serikali au Wizara ya Ujenzi mko tayari kuiachia Halmashauri ya Wilaya ya Ubungo kupanga wajasiriamali hao ili kufikia malengo tuliyotarajia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa mpaka sasa wajasiriamali wanateswa sana kupitia Wizara ya Ujenzi katika eneo lao la TANROADS katika maeneo haya waliyopo.

Je, Serikali ipo tayari kuchukua ombi la kuwaacha kipindi hiki wajasiriamali mpaka mradi utakapokamilika katika maeneo haya ya pembezoni mwa barabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Serikali nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kutambua kazi nzuri anayofanya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan. Nasema tu kwamba, kwa kuwa tunaowalenga ni wajasiriamali wa eneo husika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatafuta mpango mzuri ambao utahakikisha kwamba wale walengwa ndiyo wanaopata vibanda hivi. Ofisi ya Mheshimiwa Mbunge mhusika tutahakikisha kwamba inashiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, naomba tu kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kikubwa ambacho hapa tunaangalia ni kulinda usalama wa hawa wanaofanya biashara. Tunaweza tukawaacha wakaendelea kufanya biashara, lakini kukatokea madhara. Hata hivyo, nasema tu tumelipokea, tutatafuta namna nzuri ya kuona namna gani wanaweza wakafanya biashara bila madhara. Ahsante. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa Jimbo la Kawe kama ilivyo Jimbo la Kibamba, lina wajasiriamali wengi sana barabarani. Kwa kuwa tuna barabara yetu kubwa kutoka Mwenge – Bagamoyo, kwa nini mpango huo mzuri wanaofanya Kibamba wasiulete pia Jimbo la Kawe ili wajasiriamali waweze kupangwa vizuri?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja tu ni kwamba, eneo hili la barabara hata wakati wa design yaani wakati inafanyiwa usanifu, hivi vibanda vinavyojengwa vilikuwa tayari viko kwenye usanifu. Sasa, itategemea na barabara kutoka Mwenge – Tegeta – Bagamoyo kama itakuwa ina design na eneo ambalo unaweza ukaweka vibanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tulichukue hilo kwamba katika barabara nyingi zinazodizainiwa mjini basi ni vyema suala hili la kuweka vibanda liwe limefanyiwa usanifu. Lisipofanyiwa usanifu halitawezekana kufanyika, ahsante.

WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya maswali ya Waheshimiwa Wabunge. Katika kuongeza jibu alilojibu Mheshimiwa Waziri, nampongeza sana Mheshimiwa Gwajima, Mbunge wa Jimbo la Kawe, kwa namna ambavyo anapambana. Hapa kabla ya swali, amekuja kuniona kuhusu changamoto ya mafuriko ambayo ipo Barabara ya Mwenge kwenda Bagamoyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemuahidi Serikali kupitia Mheshimiwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, tutakaa na kujipanga ili tuweze kwenda site na kuona cha kufanya ili kuwatoa wananchi kwenye adha ambayo Mheshimiwa Gwajima ameitaja. Ahsante sana.
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniruhusu kuuliza swali moja la nyongeza. Mheshimiwa Waziri, nakumbuka tulisaini Mkataba wa Barabara ya Mwendokasi inayoanzia Mwenge – Tegeta – Basihaya. Je, ni lini barabara hiyo ambayo Mkataba wake tumeshasaini itaanza kujengwa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba tu kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri siku ya kusaini hiyo barabara mimi mwenyewe nilishiriki. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hatua iliyopo sasa hivi iko kwenye zile hatua za awali, yaani mobilization kwa ajili ya kuanza kuijenga hiyo barabara. Wakandarasi tayari wako wanafanya mobilization kwa ajili ya kujenga, yaani maandalizi ya awali kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hiyo, ahsante.

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kama ambavyo ilivyo Kawe, Barabara ya Mafinga – Mgololo ambayo tulisaini Tarehe 26 mwezi Juni. Wananchi wananiuliza na juzi nilikuwa pale Kanisani pale Bwawani kwa Mzee Mahimbi, Wachungaji wakanivuta pembeni wakasema hii barabara inaanza lini? Ninayo majibu lakini wananchi wangetamani kusikia majibu ya Serikali.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Mafinga – Mgololo ina urefu wa kilometa 81 na ni kati ya zile barabara ambazo zinatekelezwa kwa Mpango wa EPC+F. Hii barabara ndiyo ambayo ni ya kiuchumi ambayo karibu sehemu kubwa ya magogo na mbao zinapita kwenye hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kumhakikishia kama nilivyosema kwenye swali la msingi la Mheshimiwa Flatei, tayari wakandarasi wako site wanafanya usanifu wao wa kina na tunategemea kuanzia Januari watakuwa wameanza kazi hiyo. Kwa sasa wako wanaandaa maeneo ya kuchukua materials, maeneo ya kujenga hizo site zao na kama kutakuwa na uwezekano wa kuigawa hiyo barabara mara mbili ili waweze kuifanya hiyo kazi kwa uharaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, mradi huo upo na tayari wakandarasi wapo site japo hawajaanza ile earth work, yaani kazi ya kuanza kuchimba Barabara, lakini wako wanafanya maandalizi, ahsante.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa nimshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri aliyoyatoa sasa hivi.

Je, Serikali inasema nini katika kufuatilia utendaji katika mizani ili kupunguza msongamano wa malori barabarani?

Swali la pili, nini mkakati wa muda mrefu wa upanuzi wa barabara kiwango cha njia, hasa barabara kuu ziingiazo nchini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi, kwamba moja ya maeneo ambayo yameonekana yanakuwa na msongamano mkubwa ni kwenye mizani. Utaratibu ambao sasa tumeanza kuufanya, kwanza ni kubadilisha mizani ile ambayo ilikuwa siyo ya kieletroniki ambayo inatakiwa gari lisimame ndiyo lipime. Sasa tunatumia mizani ambayo tunasema weigh in motion yaani gari linakuwa linatembea huku linapima, kwa hiyo litumia muda mfupi sana, ikiwa ni pamoja na kuweka mizani pande zote mbili. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo kwenye mizani hiyo kumepunguza sana changamoto ya msongamano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mpango wa kuzipanua barabara kwenye mipaka yetu ama njia zinazoingia nchini, ziko barabara hasa kwenye vituo vyetu vya forodha vikubwa kama Tunduma, ambako sasa hivi tunafikiria namna ya kuongeza njia kutoka njia mbili kwenda njia nne ili kupunguza msongamano katika maeneo hayo. Ndiyo maana katika mradi wa sasa ambao unakwenda kwa mfano mpaka wa Tunduma, barabara inayojengwa ni ya njia nne. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, ni lini barabara ya mchepuo katika Mji wa Njombe kutoka Kibena kwenda mpaka maeneo ya Kobe itaanza kujengwa kuondoa adha ya malori?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Sasa hivi kilichofanyika katika Mji wa Njombe ambao Mji unakua kwa kasi sana, wameshafanya usanifu wa awali kabisa (reconnaissance survey) ili kuona namna wapi barabara ya mchepuko itapita katika Mji wa Njombe. Kwa hiyo mipango hiyo ipo kinachofatia sasa hivi ni kutafuta fedha kukamilisha huo usanifu. Ahsante.

MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kuniona. Niipongeze Serikali kwa kutenganisha Wizara ya Ujenzi na Wizara ya Uchukuzi.

Kwa kuwa, vyombo vya usafiri barabarani vimeongezeka, ukianzia baiskeli, bajaji, bodaboda, magari madogo mpaka malori lakini barabara hizo zimebakia ni zile zile mbili. Nikifatilia majibu ya msingi ya Mheshimiwa Waziri amezitaja zote kwamba zitapanuliwa lakini mimi nauliza kabisa, ni lini haswa Barabara ya kutoka Dar es Salaam mpaka Arusha - Namanga na inayokwenda mpaka Cape Town itapanuliwa ili basi ianzie hapo tuende ile ya Dar - Mbeya, Dar - Lindi, Dar – Mwanza, Dodoma - Arusha?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakiri kwamba barabara nyingi ambazo tulijenga zamani, zilijengwa kulingana na mahitaji ya wakati huo na lazima tukiri kwamba tunapoona magari mengi yameongezeka maana yake uchumi wetu, umezidi kukua na ndiyo maana tunaona magari makubwa na malori makubwa. Kwa hiyo, sasa hivi tunachofanya hizi barabara zote tunapotakiwa kuzipanua ni kwamba ni lazima tufanye usanifu upya, halafu tuzijenge kwa kiwango cha sasa. Kwa hiyo Serikali imeliona hilo ikiwa ni pamoja na barabara hiyo ya kutoka Chalinze kwenda Mombo hadi Moshi. Kwa hiyo, tayari zimeainishwa, kinachotegemewa sasa ni kutafuta fedha ili kuanza kuzitengeneza hizo barabara mpya kwa kiwango cha sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana hata sasa barabara tunazozijenga upana wake ni tofauti kabisa na upana wa barabara zile zilizojengwa zamani ikiwepo barabara aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge., Ahsante sana.
MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa, msongamano uliopo Mji wa Tunduma ni mkubwa sana na katika hali ya kawaida upanuzi wake utakuwa gharama kubwa sana, bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri alipita akaona uwezekano wa kujenga barabara kiwango cha lami kuanzia Laela kwenda kuunganisha ile barabara kwenda Kasesha.
Je, nini mpango wa Serikali katika kuondoa msongamano huo?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza tu niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba pamoja na mchango wa barabara kuleta msongamano Tunduma lakini kuna mambo mengine ambayo ni ya kiforodha ambayo yanasababisha msongamano katika Mji wa Tunduma ikiwa ni pamoja na wenzetu wa upande wa pili ambao hawaendani na kasi ya kwetu. Sisi tunafanya masaa 24 wao wanafanya masaa 12.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kumjibu Mheshimiwa Mbunge, ni kwamba tunafikiria kama Serikali kwanza kutengeneza bypass kutoka Mpemba kwenda kuunganisha na barabara inayokwenda Sumbawanga ili magari ambayo yanaenda njia ya Sumbawanga yasilazimike kupita Tunduma, hilo la kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kweli nimepita kwenye barabara aliyoisema ambayo kama tutaijenga kwa kiwango cha lami itasaidia sana magari mengi kwenda Bandari ya Kasanga ikiwa ni pamoja na mpaka wa Kasesya. Kwa hiyo, hiyo mipango ipo kinachosubiriwa tu ni Serikali itakapopata fedha kuijenga hiyo Barabara. Ahsante.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa unatoka Kibaha unaenda Dar es Salaam kwenye njia nane, kuna Maliasili Idara ya Misitu wanakagua malighafi za misitu kwenye hiyo njia nane barabarani kabisa, kitu ambacho kinasababisha msongamano na ajali.

Ni kwa nini Serikali isiweke mchepuko kama wanavyofanya kwenye mizani waweze kuwajengea wakifika pale wanachepuka, wanakaguliwa, wanaingia kwenye highway wanaendelea, kuliko kukaguliwa kwenye high way?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nilichukue suala hilo kwa ajili ya kulifanyia study na kuona uwezekano wa hicho alichokisema Mheshimiwa Esther Matiko Mbunge. Ahsante.(Makofi)
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona.

Hivi karibuni tulisaini mkataba wa Barabara ya Sengerema - Nyehunge kwa kiwango cha lami na Mheshimiwa Naibu Waziri alikuwepo lakini imekuwa kimya. Je, tunaweza kufahamu tatizo hasa ni nini mpaka muda huu kazi hiyo haijaanza?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge Eric Shigongo, kwamba tulisaini mkataba lakini maendeleo ni madogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tayari Mkandarasi huyo ameshaitwa na Wizara na Mheshimiwa Waziri kujua changamoto yake ni nini ili tuone taratibu za kuchukua za kimkataba kama itaonekana kwamba huyo Mkandarasi ana changamoto ili taratibu za kimkataba ziweze kuchukuliwa, ili tuone kwamba hii kazi nzuri anayoifanya Daktari Samia isikwamishwe na huyu Mkandarasi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshaliona na hatua tayari tumeshaanza kuchukua. Ahsante.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Barabara hii imesainiwa tarehe 19, ni zaidi ya mwezi mzima tangu imesainiwa. Je, ni lini mkandarasi atakabidhiwa site ili aanze kazi rasmi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Barabara ya Omugakorongo – Kigarama mpaka Mrongo ilitangazwa kujengwa kwa kiwango cha lami, lakini mpaka sasa hivi haijulikani ni hatua gani imefikia ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kyerwa kwamba, baada ya kusaini barabara hii kinachofuata sasa ni kumkabidhi mkandarasi ili aanze kazi. Tayari Meneja wa Mkoa wa Kagera ameshapewa maelekezo na TANROADS Makao Makuu kwamba kuanzia tarehe 5 mwezi huu, siku yoyote huyu mkandarasi aweze kukabidhiwa kazi na aanze kazi.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la Barabara ya Omugakorongo – Murongo, ilikuwa tayari imeshapata mkandarasi, lakini kwa taratibu za kimkataba, yuko mkandarasi ambaye ali-appeal, yaani alipinga mchakato wa manunuzi na hivyo imeamuliwa kazi hiyo itangazwe tena. Kwa hiyo, tuko kwenye hatua nyingine ya manunuzi baada ya ule mkataba wa kwanza kuonekana kwamba ulikuwa na changamoto za kisheria. Kwa hiyo, taratibu zinaendelea, tayari tuko kwenye manunuzi tena. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Barabara ya Masasi mpaka Liwale, kilometa 175, ni barabara ambayo imesainiwa tarehe 16 mwezi wa Sita mwaka uliopita 2023 kuwa itajengwa kwa EPC+F, lakini barabara hii usanifu wake …

SPIKA: Mheshimiwa Kuchauka, uliza swali.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, wana-Liwale wamenituma niulize, barabara hii ujenzi wake unaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, barabara aliyoitaja itaanza kujengwa mwaka huu kama tulivyokuwa tumeahidi. Ahsante.

SPIKA: Mwaka huu ukimaanisha 2023/2024 au 2024/2025?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, tunategemea kuanza ujenzi wa barabara hiyo mwaka huu wa fedha.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Mkataba wa Ujenzi wa Barabara ya Ruaha National Park utasainiwa?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, Barabara ya Iringa – Msembe – Ruaha National Park, sasa hivi tuko kwenye evaluation na inafadhiliwa na World Bank. Baada ya kukamilisha taratibu hizo, barabara hiyo itaanza kujengwa. Ahsante.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, Serikali ina kauli gani kwa barabara ya Iringa (MR) – Pawaga Road (Itunundu) ambayo mkandarasi ametelekeza vitu na haendelei na wakati alikuwa ameichimbachimba, hivyo wananchi kupata shida?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Mbunge, baada ya hapa tuweze kukutana naye ili niweze kujua changamoto ya huyo mkandarasi na tuweze kuondoa hiyo changamoto ambayo mkandarasi anaileta kwa wananchi. Ahsante.

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, je, ni lini Barabara ya bypass inayoanzia Kata ya Kisaki mpaka Mtipa itaanza kujengwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ilishasanifiwa na Serikali kwa kweli inaendelea kutafuta fedha ili kuweza kuijenga hiyo Barabara ya Bypass katika Mji wa Singida.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, ni lini ujenzi wa Barabara ya Mbagala Rangi Tatu mpaka Kongowe ambayo ipo katika bajeti ya mwaka huu utaanza?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hiyo kilometa 3.8 imeshapata kibali cha kutangazwa ili ianze kujengwa. Ahsante.

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, Barabara ya Kongwa – Kiteto – Simanjiro ni lini itaanza kujengwa?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, hiyo ni barabara ambayo iko kwenye EPC+F. Kama nilivyosema, tunategemea hizo barabara zianze kujengwa mwaka huu wa fedha. Ahsante.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, naomba kufahamu, je, Serikali imefikia hatua gani kwenye maandalizi ya kujenga barabara ya Hydom – Mogitu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ilishafanyiwa usanifu na tayari Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Spika, ni lini Barabara ya Iguguno – Nduguti, Wilaya ya Mkalama itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hiyo itaanza kujengwa mwaka huu, lakini imeshapata kibali cha kuitangaza. Kwa hiyo, bado tunatangaza, lakini tuko kwenye hatua ya kuitangaza mwaka huu. Ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru, ni lini barabara ya Utegi – Shirati – Kilongwe itaanza ujenzi kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, barabara hii ndiyo kati ya zile barabara za kilometa 27 ambazo zimepewa kibali itangazwe kwa ajili ya kuanza ujenzi. Ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, ni lini Barabara ya Kongwa – Mpwapwa itaanza kujengwa?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Spika, tayari mkandarasi alishapatikana, kwa hiyo, kinachosubiriwa sasa hivi ni kumkabidhi site. Ahsante.