Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kutoa hitimisho la hoja ya Mpango na Makadirio ya Matumizi ya fedha ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa mwaka huu wa 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru sana Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mheshimiwa Mhandisi Dkt. Leonard Madaraka Chamuriho kwa ushirikiano mkubwa anaonipa ambao umeniwezesha kutekeleza majukumu yangu ya Unaibu kwa urahisi. Pia namshukuru Naibu mwenzangu hapa kwa jinsi tunavyoweza kushirikiana katika kumsaidia Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi niweze kujibu hoja mbalimbali ambazo zimejitokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge kwenye eneo la barabara wameongea kwa hisia kali sana. Ni kweli mahitaji ya barabara na hasa kwa kiwango cha lami, ni makubwa sana. Tukirudi nyuma miaka michache tu, miaka sita, tutakumbuka miundombinu ya barabara ilivyokuwa. Hivyo, tuna kila sababu ya kuishukuru Serikali kwa awamu zote kwa jinsi ambavyo imekuwa ikifanya vizuri katika sekta ya miundombinu. Kikubwa tu ni kwamba barabara hizi ni nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge watakubaliana nami kwamba moja ya kigezo kikubwa sana ambacho kimeiingiza Serikali ya Awamu ya Tano na Wabunge wengi kupata kura nyingi sana za kishindo kilichangiwa sana na eneo hili la jinsi Serikali ilivyofanya vizuri katika sekta ya miundombinu ikiwa ni barabara, reli, bandari na viwanja vya ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niende kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, imesema nini? Ni kweli kwamba tuna ilani ambayo tunatekeleza, lakini ilani hii inatekelezwa kwa miaka mitano. Katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2020 - 2025, kilometa ambazo zimeainishwa zitajengwa kwa kiwango cha lami, kwanza zinakamilishwa 1,716, zinazojengwa ni 6,006 kwa kipindi hiki cha miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha inayohitajika kukamilisha barabara hizi ni takribani shilingi trilioni 11. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge isingekuwa rahisi barabara zote hizi ambazo zimeainishwa zikapata nafasi kwa kipindi hiki, lakini tukubali kwamba tunatekeleza barabara hizi kwa miaka mitano. Barabara ambazo zitafanyiwa upembuzi yakinifu zina kilometa 7,500; zinahitaji karibu shilingi trilioni 11.5. Kwa hiyo, ukiangalia unaweza ukaona hiyo bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijibu hoja ya mchangiaji mmoja na hasa Mkoa wa Kigoma. Mkoa wa Kigoma sasa hivi wana barabara tatu zinazoingia makao makuu. Barabara ya Kigoma – Nyakanazi wakandarasi wote wako site. Barabara inayounga Tabora na Kigoma imebaki kipande cha Malagarasi – Uvinza ambacho muda wowote kinaanza kutengenezwa. Pia Mpanda kwenda Kigoma, wakandarasi wapo wanapunguza barabara ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa nadhani ni Mkoa wa Katavi tu na Kigoma ambao wanafika Makao Makuu bila kupita kwenye lami, lakini wakandarasi wako site. Angalau mikoa yote mtu ana uwezo wa kufika Makao Makuu kupitia kwenye lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo suala lilijitokeza la muda wa barabara. Nitolee mfano barabara ya Dodoma – Iringa; tatizo kubwa ilikuwa, barabara hii ni traffic projection ambayo hatukutegemea kama barabara itakuwa na mzigo mkubwa na wingi wa magari kama hayo ambayo yamejitokeza hapo katikati, lakini ndiyo maana umepunguziwa muda ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la matuta lilijitokeza. Iko sheria ambayo imetoka, miongozo ambayo pia tunayo ya SADC ambao tunashirikiana nao, niwahakikishie Wabunge kwamba tumeendelea kutoa matuta yale ambayo hayakindi vigezo ama hayaendani na huo mwongozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia niwape comfort Waheshimiwa Wabunge kwamba barabara zote ambazo zimeathirika kutokana na mafuriko, tumejipanga; yako madaraja ya muda ambayo tumeyaagiza, tutahakikisha kwamba tunafanya tathmini na kurudishia maeneo yote ambayo yamekatika ikiwa ni pamoja na kuinua matuta sehemu ambazo zimeathirika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwa na suala la vigezo vinavyotumika kutengeneza barabara za lami, barabara ili iweze kutengenezwa kwa kiwango cha lami lazima iwe ni barabara ya ukanda, yaani barabara ambazo zinaunga kwenye ushoroba, ziwe zinaunga mikoa, barabara iwe ni ahadi ya viongozi wa kitaifa kwa maana ya Mheshimiwa Rais, Makamu ama Waziri Mkuu, iwe ipo kwenye Ilani ya Chama Tawala, iwe ni kutekeleza Mipango ya Maendeleo ya Miaka Mitano. Pia barabara zinazoenda kwenye eneo la kuchochea uchumi ambalo ni kama utalii, uzalishaji mali na vitu kama hivyo na vile vile liwe ni eneo la ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba tu, niwaombe Waheshimiwa Wabunge watupitishie bajeti ili twende tukatekeleze hiyo mipango ambayo wananchi wanahitaji sana barabara zao zikatengenezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hivyo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Waheshimiwa Wabunge sasa nimwite Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Mheshimiwa Engineer Dkt. Leonard Madaraka Chamuriho aje ahitimishe hoja yake.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba nami nianze kuunga mkono hoja hii. Nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana katika Bunge lako Tukufu ili kuhitimisha hoja ya Mheshimiwa Waziri ambayo aliiwasilisha jana. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini kwa nafasi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Waziri wangu, Mheshimiwa Prof. Makame Mnyaa Mbarawa kwa jinsi ambavyo anaiongoza Wizara, nasi wengine kwa kweli tunajivunia kufanya kazi chini yake na kupata uzoefu ambao mwenzetu kwa kweli amebobea katika Wizara hii. Tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii kuishukuru familia yangu ambao uwepo wao ndiyo unanifanya niwe na utulivu. Pia nawashukuru wananchi wote wa Jimbo la Ileje ambao wametulia na wanaamini nawawakilisha vyema. Nami nasema kwa kweli ninawakilisha vyema na wananipa ushirikiano mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu chini ya Mheshimiwa Selemani Moshi Kakoso; Makamu Mwenyekiti, Mama yangu Mheshimiwa Anne Kilango kwa jinsi ambavyo walichambua bajeti hii ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru Wabunge wote wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa michango yao. Baadhi ya hoja naamini zitatolewa ufafanuzi na Mheshimiwa Waziri, lakini mimi nitatoa ufafanuzi wa baadhi ya hizo hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan amejitanabahisha kama Rais ambaye amedhamiria kwa dhati kuifungua Tanzania. Anaifunguaje Tanzania hii? Kuna vipaumbele kadhaa ambavyo Mheshimiwa Rais anavifuata. Kwanza ni kuteleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi inaelekeza tufanye nini? Kuunganisha Makao Makuu ya Mikoa kwa lami, kuunganisha nchi na nchi, bandari zetu, barabara za kimkakati, kupunguza misongamano katika majiji na miji na pia kupeleka barabara za lami za ulinzi katika Tanzania. Kinachofuata baada ya kukamilisha huo mkakati, itakuwa ni kuunganisha wilaya zote na makao makuu ya mikoa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kitu ambacho kinafanyika na Wizara, kwanza nikutengeneza barabara ya mzungunguko wa nchi nzima kuanzia Mtwara, Songea, Nyasa, Kyela, Ileje, Tunduma, Sumbawanga, Mpanda, Uvinza na Kigoma. Ukitoka Kigoma unakwenda Manyovu, unakwenda Kasulu ama unakwenda Nyakanazi unakwenda mpaka Rusumo – Bunazi - Omurushaka – Murongo; unarudi Omugakorongo unakwenda Kyaka, Bukoba; unarudi Lusaunga, unaenda Geita - Busisi kwenye daraja letu kubwa unavuka unaenda Kigongo - Mwanza – Musoma; Musoma - Nata unaingia kwenye Mbuga, unakwenda Arusha; Arusha unazunguka Mlima Kilimanjaro kwa lami, unakuja Himo unaweza ukaamua kwenda Same, ukaenda kwa Mheshimiwa Mama Kilango sasa ama Korogwe, unaenda Tanga; Tanga – Pangani – Makurunge – Bagamoyo - Dar es Salaam – Mkuranga - Lindi, uko Mtwara tayari kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hivyo vipande, kipande ambacho hakina mkandarasi sasa hivi, lakini viko kwenye hatua katika hizo nilizozitaja ni kutoka Kyela kwenda Ileje, lakini soon tutatangaza, alichosema kuanzia Mpanda kwenda Mishamo, mkandarasi yupo na tunategemea kupata fedha kutoka Mishamo kwenda Uvinza hadi Kanyani. Kasulo kwenda Bugene tayari tuna mkandarasi yuko pale, kwa kaka yangu Bilakwate soon Mheshimiwa anakwenda kuandika mkataba. Ukitoka Murongo kuja kwa Omugakorongo tayari tuko kwenye hatua za manunuzi. Mheshimiwa Rais ameamua kuifungua nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema nitatoa mfano mmoja ni namna gani Mheshimiwa Rais anakwenda kupunguza misongamano katika miji na hasa majiji. Nitaongelea Jiji la Mbeya ambalo waliopita kwa kweli ni mtihani kwa sasa. Mheshimiwa Rais kwanza alitoa kilometa 29. Ulikwenda ukasema barabara inaning’inia, inaishia Ifisi, kwa nini isifike airport? Mheshimiwa Rais anaongeza kilomita nne, ziko kwenye manunuzi. Pia ameirudisha kutoka Uyole kuja Mlima Nyoka, badala ya 29 sasa ni 37. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu Mji wa Mbeya ni mfinyu, wananchi wa Mbeya waelewe kwamba ile barabara ambayo inapitika sasa itakuwa ndiyo diversion. Kwa hiyo, kulia zinajengwa barabara mbili na hiyo barabara ya sasa baadaye ndiyo itatumika kama barabara ya mwendokasi kwa Miji wa Mbeya. Barabara yote sehemu kubwa itawekwa taa pamoja na vivuko na kwa watembea kwa miguu. Huyu ndio Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anavyotaka kuipanga miji yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sitaki kuongelea Dodoma, wanaotembea wanaona kinachofanyika. Barabara kwa Dodoma tuna mzunguko wa nchi ambao tunajengwa, tuna mzunguko wa kati, tuna mzunguko wa ndani. Huo ndiyo utakuwa Mji wa Dodoma, lakini kwa kaka yangu hapa tutajenga Songea Bypass. Kwa African Development kwa fedha ya World Bank. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka tu niseme baadhi ya mambo ambayo yanafanyika. Hapa katikati, barabara za EPC ambazo zinatembea hapa katikati kuanzia Songea kwenda kwa kaka yangu Mgungusi pale Malinyi mpaka Ifakara tunakuja mpaka Mikumi, mpango sasa ni kujenga barabara ya kutoka Mikumi kuja Kilosa kwa kaka yangu Mheshimiwa Profesa Palamagamba ili mtu akitoka Songea anakuja Dodoma anatoka Mikumi anakuja Kilosa anakuja Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutoka Kongwa – Kibaya - Orkesumet kwa kaka yangu Mheshimiwa Ole-Sendeka mpaka Arusha, lakini tunaanzia Kiberashi tunakuja Kibaya - Chemba – Kwamtoro – Singida, barabara ya Tanga ameishaifungua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unavyoona magogo yote haya yanatoka Mgololo, EPC + F inaanzia Mafinga kuchukua ambako mpaka sasa hivi ni barabara ya changarawe kuijenga kwa kiwango cha lami kwa kutumia mtindo huu wa EPC + F. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kaka yangu Mheshimiwa Kuchauka alisimama, Mheshimiwa Ungele alisimama, kaka yangu wa Nachingwea alisimama. Barabara kutoka Masasi - Nachingwea hadi Liwale inakwenda kujengwa kwa EPC + F. Tuna barabara ambayo nataka niwahakikishie ndugu zangu wa Mtwara; Mnivata – Tandahimba – Newala – Masasi yenye kilomita 160, lot mbili; Mnivata hadi Mitesa, Mitesa hadi Masasi, saa yeyote mkataba utasainiwa. No objection imeshatolewa, kwa hiyo, tunakwenda kufungua pia huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna Barabara ya Igawa kwenda Tunduma, EPC + F na katika Mkoa wa Mbeya kutakuwa pia na Bypass ambayo itaanzia Uyole hadi Songwe ili magari makubwa hayo yasipite hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wengi wanataka nitaje barabara zao, lakini naomba nitaje barabara moja ambayo sisi kama Wizara tunaambiwa katika barabara zote zile kubwa hasa trunk road ambayo imebaki ndefu ni barabara ya kutoka Mbalizi – Mkwajuni – Makongorosi – Rungwa. Ukifika Rungwa itaenda Ipole kwa kaka yangu Mheshimiwa Kakunda ama unakuja Itigi. Hii Mheshimiwa Waziri amesema tutaitafutia utaratibu maalum, japo tumeanza kuijenga upande huku na kutoka Itigi kuja huku, Makongorosi kuja huku, lakini hilo ndilo eneo ambalo tukishajenga tutakuwa tumeunganisha sasa kusini kwenda kaskazini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maana yake ni nini? Anachokifanya sasa hivi Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, nimezungusha hizo Barabara, lakini ukitoka Nyasa – Mbinga – Songea - Njombe, utaamua ukitoka Njombe uje Iringa, unakuja Dodoma; Dodoma unaweza ukaamua kwenda Kongwa ama ukaenda Babati huko Arusha, unatoka Kenya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ukitoka Dar es Salaam kwenda Kigoma sehemu pekee ambayo sasa unaweza ukatembea kwa vumbi ni kati ya kaeneo kanaitwa Chagu – Kaizilava, bado kama kilomita 13 na Uvinza – Malagarasi ambapo wakandarasi wako site. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lile eneo ulilosema, sasa hivi tunatoka Mpanda – Luhafwe, Lohafwe – Mishamo. African Development Bank sasa hivi tupo na mpango watukamilishie barabara hiyo kutoka Mishamo hadi Uvinza. Kwa kweli tunakwenda vizuri sana kwenye miundombinu. Wanaotaka ku-google waangalie, kwenye miundombinu Tanzania sasa hivi ni wangapi? Ndiyo maana Mheshimiwa Rais hakupata hiyo tuzo kwa bahati mbaya, ni kwa sababu ya hii kazi. (Makofi)

SPIKA: Nadhani makofi hayo yanaashiria kwamba Waheshimiwa Wabunge hawana swali la nyongeza, wamesikia maelezo ya barabara zote. Kwa hiyo, nadhani wamekusikia kwa kweli. Wamekusikia Mheshimiwa Naibu Waziri, nadhani haya makofi yatakuwa yanaashiria tumekuelewa, huna haja ya kuendelea kuzungumza. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, bandari zote sasa hivi mpango ni kuziunganisha kwa kiwango cha lami. Tuna bandari tumejenga Karema, tumeishatangaza tenda Mpanda – Karema, tuna barabara ya Lyazumbi kwenda Kabwe, ipo kwenye mpango, barabara ya kutoka Sumbawanga – Matayi hadi Kasanga imeshakamilika. Bandari hizi zote tumeshazijenga. Pia tuna barabara ambazo zinaunganisha na nchi ambazo bado. Moja ya barabara hizo ni Likurufusi – Mkenda barabara ambayo muda wowote kuanzia sasa hivi tutaitangaza kilomita 60 kuanzia Likurufusi hadi Mukulu kilomita 60. Mkataba upo tayari kwa ajili ya kusainiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara za kutoka Songea kuja kuunganisha na Mkoa wa Njombe ziko tayari kusainiwa na nyingine wakandarasi wako site. Sasa hivi tunajenga barabara kwa kiwango cha zege kutoka Njombe kwa maana ya Itoni – Lusitu – Mawengi kuja Manda. Barabara ni bora kabisa katika Afrika kwa kiwango cha zege. Tumeshakamilisha kilometa 50, tunaendelea kujenga kilometa 50. Tuna barabara ambazo zinaunganisha Mkoa wa Njombe kupitia Makete kuja Isyonje kuunganisha na Mkoa wa Mbeya, wakandarasi wako site wanafanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna barabara inatoka Kyela - Katumba Songwe – Ngana – Ikinga – Ibungu – Isongole, mkandarasi muda wowote anakabidhiwa site aanze kujenga kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, lakini siyo kwa umaana, Mkoa wa Arusha tumepata maelekezo maalum. Baada ya Royal Tour kiwanja cha Lake Manyara kimeshalipiwa fidia, tunaanza kukijenga, lakini kutokea hapo hapo Lake Manyara ambapo ni Karatu, tunajenga EPC kutoka Karatu kuja Mbulu – Haydom – Idarafa – Sibiti – Lalago hadi Maswa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile Barabara ya Mto wa Mbu – Engaruka – Oldonyo Lengai – Sale hadi Waso ambapo unakuwa upo kabisa kwenye Klein’s Gate ya Serengeti tumeshakamilisha kilomita 40 na maelekezo yametolewa maalum kwenye maeneo yote korofi kuna kilomita kama 39 tujenge kwa kiwango la lami.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, ahsante sana. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kuchangia hoja ya Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Bunge, hasa ya Miundombinu.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Kamati ya Miundombinu wakiongozwa na Mheshimiwa Selemani Kakoso na Makamu wake Mheshimiwa Anne Kilango na Wajumbe wote kwa jinsi ambavyo wanatushauri sisi kama Wizara na kutoa maelekezo.

Mheshimiwa Spika, bila kupoteza muda, naomba sasa nijielekeze kwenye mchango wangu hasa kutokana na maoni ya Kamati. Nilisikia Kamati kwamba karibu mambo yote ambayo walikuwa wametuelekeza tunaendelea kuyatekeleza, nami nataka nitoe mchango kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu muundo wa TBA ili iweze kufanya na sekta binasfi; Machi, 2022 wakati Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anazindua Mogomeni Quarter, moja ya jambo ambalo analieleza, ni kueleza Wizara na TBA kwamba waangalie uwezekano wa TBA kufanya kazi na sekta binafsi. Hivi ninavyoongea, tayari muundo wa TBA umeshakuwa reviewed kwa maana ya establishment order, pamoja na majukumu yake yote ambayo ilikuwa inayafanya, lakini pia sasa itaanza kufanya na sekta binafsi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa hivi kwa maana ya taratibu zote tunasubiri tu baraka za mamlaka ambayo ndiyo ilitoa hayo maelekezo pamoja na Kamati ya Miundombinu. Hivyo, tuna uhakika suala hili liko mwishoni na itakuwa hivyo, kufanya kazi na sekta binafsi ikiwa ni pamoja na majukumu yake yote iliyokuwa inayatekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, limejitokeza pia suala la TANROADS kuachia kazi kwenda TAA. Nataka kulijulisha Bunge hili kwamba hilo suala pia wataalam wameshashauri. Ni kweli kwamba TANROADS itaachia shughuli zote kwenda TAA lakini kwa hatua. Kwa sababu gani? Kwa sababu shughuli zote ambazo zilikuwa zimeingiwa mikataba na TANROADS, zitaendelea kufanyika kwa sababu ya mikataba yake, huku kama walivyoshauri wataalam, TAA ikianza kuchukua kazi.

Mheshimiwa Spika, sisi kama Wizara, kwa sababu taasisi zote ziko chini ya Wizara, hilo tumeshalikubali na litakwenda kutekelezwa hivyo, lakini kwa muda ili tusije tukaathiri miradi ambayo inaendelea ambapo tayari TANROADS walishaingia mikataba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu TEMESA, tayari Kamati ilishashauri kwamba Serikali iangalie muundo na utendaji kazi wa TEMESA na Serikali inaendelea kulifanyia kazi hilo. Kwa hiyo, nataka nilihakikishie Bunge hili kwamba tunaendelea kulifanyia kazi kama alivyoshauri Mheshimiwa Dkt. Ndugulile. Tayari Serikali ilishaliona na Kamati ilishashauri na tayari kazi inaendelea kuunda upya majukumu yake na muundo wake ili kuleta tija.

Mheshimiwa Spika, suala la fidia ya Itoni – Lusitu – Mawenge – Ludewa hadi Manda; ninapoongea sasa hivi, ni mama mmoja ambaye hajapata ambaye hakuwepo, na mtu mmoja, nyumba Na. 45 Kijiji cha Mlangali ambaye baada ya realignment alisahaulika, lakini fedha yake ipo na atalipwa wakati wa kulipa watu wa kati ya Mradi wa Itoni kwenda Lusitu ambapo jedwali liko tayari. Kwa hiyo, tumetekeleza yale maagizo ya Kamati.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Hazina kuipatia fedha TBA; kwa kweli kwa sasa Hazina imeendelea kutoa fedha nyingi na ndiyo maana tunaona sasa hivi majengo mengi TBA yanajengwa, pamoja na ruzuku ambayo TBA wanaitoa ya kujenga majengo kwa ajili ya wafanyakazi na nyumba za Serikali.

Mheshimiwa Spika, mwisho, kuhusu bajeti…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, utakubaliana nami kwamba katika kipindi ambacho Serikali inalipa wakandarasi, ni kipindi hiki. Ndiyo maana miradi mingi inakwenda. Hata ukiwauliza wakandarasi, kwa kweli ni tofauti na ilivyokuwa na ndiyo maana miradi mingi inalipwa. Kadri tunavyotengeneza certificate kwa kweli Wizara ya Fedha inalipa na ndiyo maana tumekuwa kati ya Taifa ambalo yanafanya vizuri sana katika miundombinu kwa Afrika Mashariki na hasa miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Spika, mwisho, kuhusu madeni ya TBA, tayari pia lipo kwenye ngazi za juu kwa maana ya kwamba wale wadaiwa sugu na hata taasisi ndani ya Serikali, mpango umeandaliwa kati ya Wizara ya Ujenzi, Wizara ya Fedha na Ofisi ya Mwanasheria Mkuu kuona namna bora ya madeni yote yaweze kulipwa. Kwa hiyo, nina hakika hili nalo litafanyika ili kuipa uwezo TBA kupata madeni yake kwa ajili ya kuiimarisha kuweza kutimiza majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. Ahsante. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Hebu tusaidie kufafanua moja lile la uwezo wa kampuni za hapa nchini kuweza kutengeneza meli na kutengeneza vivuko halafu zisiweze kukarabati. Au ni ule utaratibu wa sheria yetu kwamba mlifanya hiyo International Competitive Tendering, kwa hiyo, akashinda yule? Hebu tueleweshe vizuri hapo.

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Moja ulilolisema ndiyo hilo kwamba mikataba mingi huwa inatangazwa kwa maana ya kwamba iko wazi Kimataifa na mtu yeyote anaweza aka-tender. Pia tuna kampuni za Tanzania ambazo kwa kweli siyo nyingi.

Mheshimiwa Spika, moja ya kampuni ambayo inafanya vizuri sana ni Songoro Marine, Iakini tunaona kazi nyingi ambazo anazifanya kwa sasa hivi ni nyingi sana.

Nasi ni kati ya watu ambao tunam-promote sana. Kwa hiyo, kutokana na hilo tukaona pengine atachelewa zaidi kwa sababu ya taasisi yake na watu alionao. Kwa hiyo, naamini kwamba kama tungempa hiyo kazi pengine angeweza kuchukua muda mrefu kuifanya. Ila ni tenda iliyotangazwa kwa maana ya kwamba iko wazi kwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia hoja hii.

Kwanza nianze kwa kuwapongeza Wenyeviti wote wa Kamati zote tatu kwa taarifa zao. Niseme tu kwamba mapendekezo yote yanayohusu Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi tumeyapokea na tunaahidi kwamba tutayafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe ufafanuzi kwa maeneo mawili ama matatu kulingana na muda na naomba nianze na eneo la kurejesha majukumu ya ukarabati, ujenzi na kazi zote za viwanja vya ndege kutoka Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) kwenda Mamlaka ya Viwanja vya Ndege.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikubaliane na Waheshimiwa Wabunge, CAG, Kamati ya Miundo Mbinu lakini pia na Kamati ya PAC. Niwajulishe Waheshimiwa Wabunge kwamba tayari kazi hiyo imeshaanza na niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge kwamba shughuli za TAA kwenda TANROADS zilikuwa ni presidential decree na hii ilikuwa ni baada ya kuona shughuli nyingi wakati ziko chini ya TAA zilikuwa haziendi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tayari wataalam wameshatoa mapendekezo ya namna ya kuhamisha majukumu kutoka TANROADS kwenda TAA kwa hatua kwa sababu ziko kazi ambazo tayari zinaendelea na hatuwezi leo tukaziondoa ghafla. Kitakachoweza kutokea kama tutakifanya hicho, ndio kama walivyosema baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kwamba kuna viwanja vilisimama kwa sababu wakati TAA inatekeleza hiyo miradi ama imeshaingia mikataba tukafanya mabadiliko. Kwa hiyo tutahakikisha hilo halifanyiki na wataalam wameshatoa mapendekezo yao, hatua za kuanza kuchukua, hatua baada ya hatua na tunategemea kwamba zile fedha ama zile kazi ambazo zitafanyika kwa fedha hasa ya Tanzania kwa maana haina wahisani, miradi yote tutakayoanza kutekeleza itaanza hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waheshimiwa Wabunge wengine watakuwa mashahidi kwamba hata sasa hivi tumeanza, pale ambapo kunakuwa na kazi wote wanakuwepo kwa ajili ya kuanza taratibu ya kuwajengea uwezo na uzoefu. Hilo kwa upande wa Serikali halina tatizo, tumeshalifanyia kazi na tunaamini kadri tunavyokwenda shughuli zote zitahamia TAA.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu bado vile viwanja vyote tulivyovijenga kama Msalato, Songea vimejengwa na hawa TANROADS na wataalam kwa hiyo tunategemea baada ya hapo pia kutakuwa na kuhamisha wataalam ambao wamepata uzoefu kutoka TANROADS kwenda kule TAA ili kuwajengea uzoefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala lingine ambalo kuna Mbunge amelichangia kwa nguvu kuhusu TEMESA. Tunatambua hii taasisi ni muhimu sana kwa sababu ndio inayoshughulikia magari ya Serikali ya Viongozi lakini pia na vivuko. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali inapitia hii Taasisi na majukumu yake ili iweze kufanya kazi vizuri zaidi. Kwa hiyo, tumelipokea Kamati ilishauri, lakini pia Wabunge wameshauri na wameendelea kushauri na sisi tunasema tumeshaona kwamba, kuna haja kubwa ya kuangalia muundo wake, majukumu yake na utendaji wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho ilikuwa ni taarifa na mapendekezo ya kiufundi na ufanisi. Nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara tunaangalia na kuweka mifumo imara sasa hivi ya jinsi ya kuangalia upungufu unaojitokeza wa kiufundi na hasa ya kiuhandisi yanayosababisha baadhi ya kazi zetu kufanyika chini ya kiwango. Niwahakikshie Waheshimiwa Wabunge kwamba, tumeliona hilo, tumelichukua, lakini tumeshaanza kuweka mifumo ambayo itahakikisha kwamba tunazuia hilo lisitokee na pale ambapo linatokea, hatua kubwa sana zinachukuliwa za kisheria na kinidhamu kwa wale ambao watakuwa wamesababisha kufanyika kwa kazi za kiufundi chini ya kiwango kama ambavyo ripoti imesema na tarifa ya PAC imesema.

Mheshimiwa Naibu Spika, masuala mengine ambayo yameongelewa hasa ya ulipaji wa certificate, Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameelezea vizuri, kwa hiyo hilo naomba nisilieleze tena.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuunga hoja ya bajeti hii, bajeti ya wananchi, bajeti ambayo kwa kweli imewasilishwa kwa umakini mkubwa na kwa umaridadi mkubwa sana, hongera sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kutoa ufafanuzi kwa mambo machache ambayo yamejitokeza kutoka kwenye michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge na hasa ile ambayo iligusa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na hasa Sekta ya Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza kupokea na kuwashukuru Wabunge wote ambao wamesimama na kuchangia, kupongeza jitihada na juhudi kubwa ambazo zinafanywa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania jinsi anavyofanya, kuitendea haki Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika sekta ya miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme hili linafanyika kutokana na ukweli kwamba Mheshimiwa Rais ametambua kwamba uchumi wa Tanzania unaendelea kukua sana na ili uendelee kukua moja ya kigezo kikubwa sana ni kufanya miundombinu na hasa barabara iwe bora ambayo inaweza ikapitika kwa uharaka na kwa urahisi na hivyo kushusha gharama ya uendeshaji hasa katika ufanyaji wa shughuli za biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunaomsaidia Mheshimiwa Rais kwa nafasi hizi, napenda tu kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge na Watanzania kwamba miradi yote ambayo tumeiahidi, tumeitangaza na ambayo tunaendelea kuitangaza, tuna uhakika kwa asilimia 100 kwamba itatekelezwa kama ilivyopangwa, kwani hatuna mashaka na yale ambayo ni makusudi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba ushauri, maoni na mapendekezo yote ambayo mmeyatoa tumeyachukua na tunaahidi kwamba tutaenda kuyafanyia kazi ili kuendelea kuboresha katika utekelezaji wa majukumu yetu katika Wizara yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nigusie suala moja ambalo kuna Mheshimiwa Mbunge ameliongelea na hasa barabara za Kigoma pamoja na miradi ile complementary projects. Mkoa wa Kigoma na Mkoa wa Katavi ndiyo mikoa ambayo kwa kweli ilikuwa haijaunganishwa na lami kati ya mikoa na mikoa. Ambacho Serikali ya Awamu ya Sita inaifanya ni kuhakikisha kwamba Kigoma hii inaunganishwa yote kwa barabara za lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge atakuwa shahidi kwamba tunapoongea, wakandarasi watano kutoka Nyakanazi hadi Kigoma kwa maana ya Kasulu - Manyovu wako site na kwa kweli kasi ni kubwa na hasa baada ya kipindi cha mvua kwisha. Upande wa kutoka Tabora sasa hivi ukishafika mpaka Malagarasi ni lami na kipande kilichobaki, mkandarasi ameshika kasi kuhakikisha kwamba pia anamaliza tatizo lilokuwepo la kilometa 51. Kwa sasa zimebaki kilometa 51.3 ukitoka hapa Dodoma kwenda Kigoma ambazo ni za vumbi, lakini mkandarasi yuko site na upande wa Mpanda pia wakandarasi wako site.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ile ya complementary ambayo ni CSR, naomba niwakumbushe Waheshimiwa Wabunge hasa wa Jimbo la Kasulu kwa maana ya Wilaya ya Kasulu, Buhigwe na Kibondo, miradi hii itaenda kutangazwa muda wowote. Changamoto ambayo ilikuwepo ni ile ya kubadilisha miradi ama maeneo. Miradi hii inafaddhiliwa na ADB. Kwa hiyo, ukibadilisha sehemu yoyote, unaingia kwenye mgogoro, lakini tunajua sasa kwamba zile changamoto zimeshaondolewa. Mapema sana kuanzia Julai, hii miradi inaenda kutangazwa ambapo itagharimu fedha isiyopungua Shilingi bilioni 23.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nigusie kidogo Miradi ya EPC. Kuna watu wameendelea kuielezea kwa namna tofauti. Katika kipindi ambacho hatujawahi kukishuhudia ni kipindi hiki cha Serikali Awamu ya Sita kusaini mikataba ya barabara yenye Shilingi trilioni 3.7 na ushee kilometa 2,035 kwa wakati mmoja. Labda tu kwa ufupi katika mpango huu wa EPC tunasema ni dhana inayohusisha utekelezaji wa mikataba ya ujenzi, yaani EPC baina ya mkandarasi na taasisi ya umma, na kunakuwa na mikataba miwili; upande wa Wizara ya Ujenzi ni EPC na wenzetu wa fedha wanafanya F. Miradi hii ina faida kubwa sana. Moja ni kwamba zile risks zote haziko upande wa Serikali, lakini hakutakuwa na variation na hakutakuwa na extension. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, yale makubaliano mliofanya ndiyo yatakayokuwa. Pia mkandarasi huyu ana uwezo wa kugawa maeneo maeneo. Kwa hiyo, katika barabara aliyopewa anaweza kuwa na vipande hata vitano ili aweze kumaliza haraka hizo Barabara. Vile vile kwa sababu ana uhakika wa kulipwa, kinachofanyika kwa Serikali sasa kwa upande wa Wizara, kuna watu wamehoji ubora, sisi tutahakikisha kwamba yaani anasimamiwa, anajenga kwa specification zilizowekwa, anajenga kwa ubora tuliouweka, na kwa sababu design ni ya kwake, akiharibu, kwa sababu wakati wa kukabidhi ile barabara, kila baada ya hatua ni lazima atahakikiwa. Tunafanya verification, pale ambapo ameharibu, gharama ni za kwake. Kwa hiyo, hatakuwa tayari kufanya hivyo kwa sababu anajua gharama itamsumbua. Hatakuwa tayari kupoteza muda, kwa sababu anajua hata akipoteza muda, hatalipwa chochote. Kwa hiyo, tuna hakika mpango huu utakwenda kuhakikisha kwamba barabara nyingi zinajengwa kwa uharaka sana, na kwa ubora mkubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tu ndio tulikuwa hatuaanza, lakini wale wanaosoma, ni miradi ambayo wenzetu ndio wanavyotekeleza miradi yao. Baada ya hapo ni kwamba hizi barabara zitakuwa ni barabara za kawaida, hakuna uhusiano wa EPC + F na PPP, tusichanganye. Baada ya hapo, hizo ni barabara za kawaida kama barabara zilizopo. Hizi ni highway, kwa hiyo, hakuna kulipia wala kufanya nini. Cha msingi tu ni kwamba hizi barabara zitajengwa kwa haraka na zikiwa zinasimamiwa na Serikali katika kila hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliona nitolee ufafanuzi kwa sababu kuna watu walikuwa wanapotosha, labda kutakuwa na kulipia, Serikali hakutakuwa na mkono; Hapana. Suala la fedha, nina hakika Mheshimiwa Waziri wa Fedha atalielezea vizuri sana namna fedha itakavyokuwa inapatikana na inavyolipwa. Watalipwa tu pale ambapo Wizara ya Ujenzi inasema alichofanya ndicho hicho ambacho sisi tulimwagiza, kinyume chake ataambiwa abomoe kwa gharama zake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hivyo, niseme hakika tuendelee kumpatia mama maua yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa afya ya kukutana hapa katika Bunge lako Tukufu na kujadili hoja hii iliyowasilishwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kuniamini ili niweze kumsaidia katika nafasi ya Unaibu Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, sekta ya ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia nikupongeze wewe, Naibu Spika na Wenyeviti wa Bunge kwa jinsi mnavyoliongoza Bunge hili. Pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara kwa jinsi ambavyo tunaendelea kushirikiana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana kaka yangu Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu, Mheshimiwa Selemani Moshi Kakoso pamoja na Makamu Mwenyekiti wa Kamati hii, mama yangu Mheshimiwa Anna Kilango Malecela, na ninaomba tu nimhakikishie kwamba tutazingatia ipasavyo yote waliyoyaeleza kwenye Kamati kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba sasa kwa uharaka nitoe ufafanuzi wa masuala mbalimbali yaliyojitokeza sana hasa yaliyojikita kwenye sekta ya ujenzi. Labda tu niwakumbushe Wabunge kwamba mtandao wa barabara za lami wakati tunapata uhuru zilikiwa ni kilometa 1,360, ambazo ni sawa tu na barabara moja upande mmoja, kutoka Dar es Salaam pengine mpaka Mwanza, nchi nzima, lakini leo tunapoongea tuna kilometa 11,512 za lami. Hili ni ongezeko kubwa sana. Ukiangalia kama tulikuwa tuna barabara ya kutoka Dar es Salaam mpaka Mwanza halafu sehemu yote hiyo ni rough road, unaweza ukapiga hesabu leo tuna barabara kiasi gani.

Mheshimiwa Spika, wakati naangalia ramani ya barabara za India wamechora barabara ya kaskazini, kusini, mashariki na magharibi. Ukituangalia na sisi Tanzania tuna barabara sasa za lami, unaweza ukatoka kusini mpaka kaskazini, ukatoka mashariki mpaka magharibi, lakini pia tuna ring road ambapo unaweza ukaanza Mwanza, ukaenda Musoma, ukaenda Arusha, ukaenda Tanga - Dar es Salaam - Mtwara ukaja Songea, ukaja Bambabay, barabara ambazo tunazijenga; ukaja Tunduma – Sumbawanga – Mpanda - Nyakanazi mpaka Bukoba. Kwa hiyo, tunaweza tu kuona jinsi Serikali za awamu zote hizi sita ambavyo zimeendelea kutengeneza miundombinu.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan amejipambua kwamba anataka kuifungua Tanzania, na tumeona jinsi miradi yote iliyokuwa inaendelea, miradi mikubwa hakuna iliyokwama, na hata ukiongea na Wakandarasi wameendelea kulipwa na miradi mingi imeendelea kuanza.

Mheshimiwa Spika, amefungua Tanzanite, amefungua barabara kubwa ya Mpanda – Tabora, Airport Msalato, Ring Road Dodoma, na tunaona BRT zinavyojengwa na barabara nyingi ambazo zinaendelea. Kwa hiyo, tunaomba tuwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ameamua kuifungua Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kila Mbunge angependa barabara yake ijengwe kwa kiwango cha lami, lakini pia niwaeleze tu Waheshimiwa Wabunge kwamba katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka hii tumekubaliana kukamilisha kilometa 1,700 ambazo zilikuwa zinaendelea kuanza ujenzi mpya kilometa 6,000, kufanya ukarabati kilometa 1,465 lakini kufanya upembuzi yakinifu kilometa 7,540 na hasa unaweza ukapiga hesabu ukaziunganisha hizo kilometa ukaona fedha ni kiasi gani. Kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge ni kwamba siyo rahisi tukajenga barabara zote kwa wakati mmoja.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tutakwenda kujenga kwa awamu kadri ilani inavyotueleza. Moja ya mkakati ambao tunakuja nao pia hasa kwenye barabara ambazo ni za changarawe tunakubaliana kwamba katika kipindi cha bajeti inayokuja, tutaainisha maeneo yote katika barabara yale ambayo mara nyingi ndiyo yanatukwamisha kupita, tuweze kuyatengea fedha kuyakarabati. Nadhani moja ya agenda kubwa ya wananchi ni barabara zipitike kwa mwaka wote na ndiyo maana utaona katika kipindi cha kiangazi tunachokwenda, hutakuta wananchi wanalalamika kwamba tumekwama, na watapita; lakini kipindi cha masika ndiyo kelele zinakuwa nyingi. Kwa hiyo, kumbe ni kweli barabara za lami ni muhimu lakini wanachotaka wananchi, waweze kusafiri katika barabara zao mwaka mzima. Kwa hiyo, hilo nadhani tutakwenda kulifanya na litapunguza watu kukwama katika njia zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaje barabara chache ambazo tayari zipo kwenye hatua mbalimbali; barabara ya Babati – Mbulu – Hydom. Barabara hii ilitangazwa kipande cha Mbulu – Hydom kilikosa Mkandarasi, tumetangaza tender. Kwa hiyo, tender zipo zinafunguliwa na kipande kinachofuata pia tunaendelea, zabuni zipo. Barabara za Handeni – Kibirashi, lot ya kwanza tayari imeshasainiwa tarehe 11 mwezi wa Nne na Mkandarasi ni Henan Highway Engineering Group ambaye tayari anaanza kazi. Kipande cha Ifakara - Kihansi kilometa 50 ipo kwenye taratibu zinaendelea. Mkiwa - Itigi inaendelea.

Mheshimiwa Spika, Igawa – Mbeya, kutokana na changamoto ambayo tunayo katika barabara ile, Uyole – Ifisi kilometa 29 tupo kwenye maandalizi ya kutangaza tender lakini Uyole – Songwe – Bypass halikadhalika Iwambi – Bypass na barabara ya Shigamba tunaanza kufanyia Usanifu. Hii yote ni kwa sababu kweli Mbeya mizigo inapita, na ni mji mkubwa ambao pale sasa imekuwa huwezi ukapita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara ya Makambako – Njombe – Songea tayari tuna World Bank wamekubali kuanza kuijenga hiyo barabara na tuna hakika hiyo barabara sasa itajengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye vivuko. Kisorya – Lugezi – Nyakariro – Kome – Mafia – Nyamisati – Bwiru – Bukondo – Ijiga – Kihangala – Magogoni – Kigamboni – Buyaga – Mbarika, hivi vivuko katika bajeti inayokuja tunakwenda kuvinunua. Hoja ya Mheshimiwa Msongozi kuhusu Mitomoni tumeisikia, lakini mpango uliopo, tumeshapitisha huu mto, tunakwenda kujenga barabara na daraja ni sehemu ya hilo.

Mheshimiwa Spika, vimezungumziwa viwanja vya ndege vya Sumbawanga, Tabora, Kigoma na Shinyanga. Viwanja hivi vimeshapata fedha, tunachosubiri ni no objection kwa sababu tuna price adjustment, tulisanifu muda mrefu lakini kwa sasa tumeomba tuongeze fedha ili tuweze kukamilisha kwa sababu ya tulifanya usanifu, fedha AID walishatuletea na Musoma Mkandarasi yupo site.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. GODFREY KASEKENYA MSONGE): Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)