Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Kenneth Ernest Nollo (20 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kutumia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwani hii ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Bunge hili Tukufu. Vilevile niwashukuru zaidi Wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM Wilaya ya Bahi na niwashukuru wananchi wa Bahi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hotuba ya Mheshimiwa Rais inaonesha dira ya namna gani taifa letu linapotaka kwenda. Tumeshuhudia nchi yetu imefanya uwekezaji katika sekta mbalimbali. Serikali imewekeza kwenye afya, elimu na sasa inawekeza kwenye miundombinu ya reli na umeme, ni mabilioni ya shilingi yanatumika katika uwekezaji. Katika nchi yetu takribani asilimia 75 ya wananchi wetu wako kwenye kilimo, kwa maana hiyo unavyowezesha afya, elimu, ni ili uwe na productive force ambayo itaweza sasa ku-engage kwenye uchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wote tunafahamu kilimo kwa maana ya uhai wa taifa lakini kilimo tangu historia ndiyo habari ya national security. Serikali nyingi duniani zimeangushwa kwa sababu ya kulegalega na kukosa chakula. Sote tunafahamu historia ya mkate ulivyoangusha utawala pale Ufaransa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuchangia hivi na hili nasisitiza siyo kwamba tulete wawekezaji kwenye kilimo, tunataka Serikali iwekeze kwenye kilimo. Maana yangu ni kwamba tumekuwa na Benki ya Kilimo lakini bado haijawasaidia wakulima. Mchango mwingi wa wenzangu waliopita wamechangia kwamba tunaagiza kwa kiasi kikubwa ngano, mafuta lakini hata sukari yenyewe bado hatujakaa sawasawa kuhimili utoshelevu katika taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilo moja ya korosho mkulima anaiuza kwa dola moja, lakini kilo moja hiyohiyo ikishakuwa processed inakwenda kuuzwa kwa dola 20. Ireland walianza na model inaitwa vertical forward integration kwamba mkulima wa alizeti atapeleka alizeti kwenye kiwanda cha kukamulia mafuta kwa huduma ya kukamuliwa mafuta, siyo kwenda kuuza alizeti yake. Ikishatoka pale sasa ile alizeti inakwenda katika mlolongo wa kwenda kuuzwa na hela ile mkulima ndiyo anaipata. Pamoja na hilo, kwenye kiwanda kile mkulima anapata hata mashudu. Kwa hiyo, ni vyema Serikali ikawekeza hasahasa kwenye ushirika, kwamba kama tunaitumia Benki ya Kilimo tuweze kuwa-empower watu wetu kwa kuanzisha vyama vya ushirika ambavyo vitakuwa na mashine za kufanyia processing.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, suala la ngano; tunatumia takribani shilingi milioni 300 kwa mwaka, hivyohivyo kwenye mafuta. Kwa hiyo, bado soko la ndani ni kubwa kwa hiyo ni vyema sasa Serikali iwekeze yenyewe si kuleta wawekezaji kwenye kilimo. Bado tuna nafasi ya sisi wenyewe kuwekeza kama Serikali ili tupate utoshelevu wa bidhaa hizi ambazo tunaagiza kwa kiasi kikubwa kutoka nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, total importation ya chakula katika Bara la Afrika ilikuwa ni dola bilioni na zaidi kwa mwaka kwa takwimu za mwaka 2018. Maana yake nini? Maana yake ni kwamba hata soko la Afrika bado ni kubwa kwa sisi Watanzania tukaweza ku-export. Tumeshuhudia tani na tani za mchele zinapita hapa kwenda Kongo, mchele kutoka Asia unapita kwenye nchi yetu kwenda Kongo. Kongo wame-import mchele kwa thamani ya dola milioni 65 lakini fedha hizi za Wakongoman zilitoka hapa na kwenda katika Bara la Asia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwenye export. Nchi ya Vietnam ni ndogo kwelikweli katika Bara la Asia, ni nchi ya tatu duniani lakini kwa ujumla wake ina-export mchele kuliko Bara la Afrika, yaani chukua nchi zote za Bara la Afrika, ziunganishe, hazifikii kiwango cha Vietnam inacho-export. Vietnam ina-export kiasi cha 1.4 billion dollars kwa mwaka; hizo ni takwimu za mwaka 2019 lakini kwa combination ya Afrika hawaifikii Vietnam, Vietnam ni nchi ndogo sana. Niliwahi kwenda Hanoi, ukitoka kidogo kama hapa ukienda Area C tayari kuna majeruba ya mpunga. Kwa hiyo, wenyewe mpunga is everywhere lakini kama navyosema, ni aibu kwa Bara zima la Afrika kwamba tunashindwa na nchi kama Vietnam.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kilimo cha mpunga kwenye Jimbo langu la Bahi.Bahi tuliwahi kujengewa skimu na FAO na IFAD. FAOwalitujengea skimu mwaka 1997; hakujawahi kufanyika tena ukarabati tangu kipindi hicho. IFAD walitujengea skimu mwaka 2004, mvua ya kwanza ilikuja ikavunja tuta, hakujawahi kufanyika tena repair na kilimo hakiendelei katika skimu ile ya Mtita.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kuhusu Bodi ya Mikopo. Nataka tubadilishe model ya kuwafadhili vijana wetu. Vijana wetu tukiwapa hela, hela ile hawawezi kuitunza, ndani ya wiki mbili, tatu wameshazimaliza na hela zinavyotoka wengi wanajaa mjini huku kwa ajili ya kugonga bia. Sasa kwa nini tusiwe na mfumo, kwa mfano nchi ya Japan, anakuwa na kadi ya kwenda ku-swipe kwenye chakula.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itarahisisha ku-manage economy, hasa vijana wetu wasiweze kushinda njaa kwenye vyuo vikuu. Badala ya kuwapa hela washike sasa tufanye utaratibu wa ku-swipe katika huduma mbalimbali, iwe kwenye chakula, hostel, hii itarahisisha vijana wetu wasome, hata book allowance siku hizi kuna vitabu electronic, wataweza ku-swipe na kununua vitabu. Suala hili litatusaidia kwanza Watanzania wengi wapata mkopo lakini vilevile itasaidia zaidi vijana wetu waweze kusoma kwa uhakika.

Mheshimiwa Niabu Spika, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nikushukuru kwa dhati kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia mpango huu wa maendeleo wa mwaka mmoja. Awali ya yote nami niseme yapo mambo ambayo Serikali imeyaainisha inataka kufanya katika kipindi hiki cha mwaka mmoja lakini jambo kubwa ambalo tunalo pia ni tatizo ni katika hali ya usimamizi wa mipango yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue maneno aliyoyasema Profesa Kitila, lengo la mipango yetu iwe ni kuondoa umaskini. Jambo hili ukiliangalia, nimeisoma hotuba ya Waziri kwa kuirudia, nimesoma mpango wenyewe, unaona kabisa baadhi ya maeneo tunatoka katika kuondoa umaskini. Umaskini kwa maana ya the object poverty bado hatujau-address vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijikite katika Mkoa wa Dodoma. Kwanza naipongeza sana Serikali kwa uamuzi wake wa kuhamia katika Mkoa wa Dodoma, Dodoma sasa imekuwa Jiji na Mji wa Dodoma unakua. Ukilinganisha maisha yaliyopo katika Jiji la Dodoma na nje ya Dodoma kwa maana ya Wilaya zake na wananchi wake bado kuna umaskini wenyewe ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili nataka niseme, kuna Mheshimiwa Mbunge alisema bado sera zetu tunachanganya, Sera ya Mkoa wa Njombe ya Kilimo inakuwa sawa sawa na Mkoa wa Dodoma, Sera ya Mkoa wa Mbeya inakuwa sawa sawa na Mkoa wa Dodoma. Sera ya Kilimo ya maeneo ambayo mvua inanyesha sana inakuwa the same treated na Dodoma. Sisi tunasikia habari ya ruzuku ya mbolea, kwetu sisi hapa hakuna. Kwa hiyo, Ukiangalia maeneo ya Kanda ya Kati, hebu naiomba Serikali iunde sera mahususi kwa maeneo kame, iwe ni sera ya kilimo katika maeneo kame. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna umaskini mkubwa kwa sababu mvua hainyeshi. Mvua inanyesha mwezi wa kwanza, mwezi wa pili imekatika. Hata hivyo pamoja na mvua hii kunyesha, maji yanayopatikana Dodoma kipindi cha mvua ni mengi. Sasa Serikali tengeni basi hata shilingi bilioni 200 au 500 mtuchimbie bwawa kubwa la uhakika la umwagiliaji. Ile Farqwa imepigwa danadana mpaka leo. Kwa hiyo, umaskini wetu sisi umekuwa mkubwa kwa sababu hatupati mvua ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili Serikali hamlifanyi, inakuja falsafa ya Waziri wa Kilimo kwamba wanaanzisha block farming, zile ni vitone vidogo lakini kwa maana ya kuondoa umaskini katika Kanda ya Kati bado Serikali haijawekeza. Sisi mbegu hatuna, sasa hivi tunatafuta mbegu, ASA (Wakala wa Mbegu) hana mbegu ya kustahimili hapa Dodoma, hatuna. Kwa hiyo, mnavyoongea habari ya ruzuku ya mbolea sisi hapa hatuna ruzuku ya mbegu na hatuna mbegu yenyewe. Mlituletea alizeti mwaka jana yenyewe inarefuka mara tatu, yaani Dodoma bado inashida na Kanda ya Kati bado ina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilisema Mkoa wa Singida unalima alizeti, leteni kiwanda kikubwa cha shilingi bilioni 200 au bilioni 300 tuweze kuweka kiwanda cha maana pale, ili tuweze kuzalisha mafuta ya uhakika. Bado hatuja address mkoa huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naliongea hili na nataka niseme, jana ulisema na si umwagiliaji ule ambao unakuja wa kukinga hivi vibwawa vya umwagiliaji vinavyotengenezwa, tunataka umwagiliaji wa matone. Tunataka tulazimishe kwamba kila mkulima awe na heka mbili za umwagiliaji wa mtama ili tuwe na uhakika wa chakula nyumbani. Maji yanatoka mengi niliwahi kusema kuanzia Kongwa shuka yote Mpwapwa ile, njoo kwetu Bahi tuna swamp, ina maji lakini nani wa kufanya utaratibu wa maji yale tuweze kuyatumia? Kwa hiyo, bado kuna tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni katika ufugaji; nchi hii tumeamua kuchunga na sio kufuga, nchi za wenzetu Kusini mwa Afrika wale wanafuga, maana yake mchungaji anataka afuate ng’ombe zake zinakokwenda naye anaenda huko huko, zinampeleka Kusini, Mbeya anaenda huko huko, mashamba ya watu yeye anachunga humo humo, ndio tatizo ambalo bado tuko nalo nchi hii. Wizara ya Ardhi hii iliyopo ukiiuliza mwaka huu imepima mashamba mangapi kwa ajili ya wafugaji? Hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kongwa nayo mnataka muanze kuilimisha alizeti, yaani ile ranchi tena tuibadilishe iwe kwa ajili ya alizeti. Kwa hiyo, bado hau-address. Watu wameacha kulisha nyasi sasa wanalisha mifugo concentrate na mahindi utaweka humo humo na kila kitu, ng’ombe anapata kilo moja kila siku. Sasa umaskini tutauondoa namna ipi? Hata hivyo tukijinasibu tunasema Tanzania ina ng’ombe 45, ng’ombe wa aina gani? Ng’ombe ambao wamekomaa, wameshupaa misuli, hawezi kula mtu kimataifa. Kwa hiyo tu-address sera zetu, ng’ombe kweli tunao, lakini tunachunga karne hii! Bado kuna tatizo, bado sera zetu...

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kingine ambacho tumeshindwa kuelewa, tumepata Awamu ya Kwanza Mwalimu Nyerere alituwekea base nzuri sana zilikuwepo ranchi alizianzisha, kiwanda kile cha Tanganyika Packers na maeneo mengi, lakini kwa nini tunashindwa ku-copy mambo ambayo yamefanyika nchi hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme Serikali ifanye mambo machache ya kuonekana. Zimbabwe walipata shida sana ya kiuchumi, wameyumbishwa, lakini Zimbabwe mwaka jana wameweza kulima ngano ya kuwatosheleza wao na ziada wamepata, nchi ya Zimbabwe, mfano mdogo kabisa. Zimbabwe sasa upande wa Kusini mwa Afrika ndio wanaozalisha maziwa kwa uhakika, laikini wanafanyaje? Walima nyasi na wanalisha pale pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka niseme bado tuna tatizo, kwanza hatuamini katika kuendelea kupitia kilimo. Tunajinasibu kwenye madini, kwenye nini, lakini kilimo ndio kinabeba watu wetu. Asilimia 65 ya Watanzania wapo kwenye kilimo, sasa nilikuwa naangalia hapa kwenye Mpango kwa mfano, kama nilivyosema Kanda ya Kati anasema kwamba kuangalia maeneo ambayo yana tatizo la mabadiliko ya tabianchi. Vinakuja vile viprogramu vidogo vidogo vile vya kimazingira na mnaitaja Bahi kwamba tutawapelekea viprogramu vya kuhifadhi, kupanda miti, tunahitaji mtuondelee umaskini. Huko mnakotupeleka viprogramu ambavyo niseme havina maana muda wake umepita sana. Tuna umaskini mkubwa tunataka kuondoa umaskini kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nalisema hili kwa dhati kabisa; reli hii imejengwa lakini unaangalia hivi reli hii ni kwa ajili ya kupeleka mizigo Congo tu au na nchi zingine? Sisi tunabeba nini kutoka hapa kwa ajili ya ku-export? Tatizo kama nilivyosema mipango yetu ni mingi, lakini je, mipango ya kuondoa umasikini iko wapi? Ziko nchi zingine ambazo tulikuwa nao sawa, nachukulia kanchi kama Bangladesh kametoka kwenye uchumi wa kilimo sasa kako kwenye uchumi wa viwanda. Hata hivyo asilimia kubwa sasa ya Wabangladesh wengi wako mjini kwa sababu ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu Mawaziri wetu na viongozi wetu wengine jitahidini kwenda kwenye nchi hizi nyingine mkaone wamefanyaje? What is the success story? Hata hivyo nchi tu kama ya Zimbabwe kama nilivyosema wenzetu wamepiga hatua kubwa kwa maana ya kuendeleza kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nataka nimalizie; wenzangu wameongelea habari ya Presidential Delivery Bureau. Malaysia ndio nchi ambayo imefanikiwa kwa kutumia Presidential Delivery Bureau na kwetu hapa kuna shida ya ufuatiliaji. Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania anaenda nje ya nchi, anaingia mikataba, anarudi, lakini nani wa kufuatilia ile mikataba? Utekelezaji wake unasuasua. Tulikuwa na Presidential Delivery Bureau baadhi ya maeneo ambayo yalifanikiwa ni namna ya kuibana Serikali katika quarterly, kwamba kulikuwa na maelekezo ya Rais haya hapa mmeyafanyanje? Sisi nchi hii tunajuana, jambo likishakuja mnaliweka mezani wale wenzetu tulioingia nao mkataba watatuma email na haijibiwi na jambo hilo tumekuwa wazito wa kujibu ndio linakuwa limetoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninachoomba na niungane na wenzangu, tunataka Presidential Delivery Bureau irudi ili kuwe na chombo cha ufuatiliaji na kukumbusha Wizara zetu kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliingia mkataba China, sasa jambo hili Wizara ya Mifugo mmefikia wapi na hatima yake imefikia wapi? (Makofi)

Kwa hiyo, kinachokosekana ni namna gani masuala ambayo viongozi wakuu wa kitaifa aidha wanaingia mikataba wanavyokuwa nje na wakirudi hapa utekelezaji wake na ufuatiliaji wake ni kidogo. Jambo hili sasa linafanya kwamba tunaingia mikataba na watu, utekelezaji ni jambo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nikushukuru kwa dhati kwa kunipatia nafasi niweze kuchangia bajeti ya mwaka 2023/2024. Kwanza nianze kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa namna ambavyo ameendelea kupambana na kuimarisha nchi yetu, hasa katika eneo zima la uchumi. Sote ni mashahidi katika nchi za Afrika Mashariki ukiacha indicator zingine lakini sisi ndio tumekuwa na nafuu kubwa ya kuwepo na kiasi cha dola kwenye nchi yetu. Pamoja na miradi mikubwa tunayoifanya tumeweza kustahimili. Na kama nilivyosema, pamoja na upungufu tuna reserve ya dola kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi nimpongeze Waziri wa Fedha ndugu yangu Mwigulu Nchemba kwa namna ambavyo ameendelea na utekelezaji wa masuala mbalimbali ya kiuchumi, na nchi yetu imeendelea kustahimili na kuweza kuimarika katika maeneo mbalimbali ya kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nimpongeze sana Mheshimiwa Rais na Serikali kwa ujumla kwa kuamua kuirudisha Tume ya Mipango. Jambo hili limesemwa sana na Waheshimiwa Wabunge kipindi kilichopita. Kwa vyovyote vile, Tume ya Mipango ni kitu cha msingi, ni taasisi ya msingi katika kuangalia maeneo gani Serikali ifanye na kuangalia dira katika upana mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania inaongozwa na mama Samia, dira na maono ya nchi yetu yeye ndiye amevishikilia. Lakini ni wapi anaposhusha, anashusha pale kwenye Tume ya Mipango. Kwa hiyo mimi nataka niseme kwamba pamoja na kwamba sasa Tume ya Mipango imerejea utekelezaji wake uanze haraka. Kazi ya Tume ya Mipango ni kwanza kupanga, kufatilia na kufanya evaluation, kuona maeneo gani ambayo tunafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niseme kwenye suala zima la upungufu wa dola, fedha za kigeni hapa nchini. Sote ni mashahidi kwamba tuna miradi mikubwa. Ni kweli kwamba tunatumia fedha nyingi kuagiza vifaa vya ujenzi. Lakini vilevile bado tuna tatizo la kununua vyakula na hata mafuta ya kula kutoka nje ya nchi. Tunanunua sana ngano kutoka nje ya nchi kwa kipindi kirefu, tunaagiza mafuta ya kula ya kutosha kutoka nje ya nchi, mbolea, dawa na vitu vingine vyote. Suala hili linasababisha kutozalisha sisi wenyewe ili tuweze kuzuia matumizi ya dola nje ya nchi. Vilevile hatuzalishi tuweze ku-export kile tunachokizalisha katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naishauri sana Serikali; katika suala zima la uwekezaji tuendelee kuweka mazingira mazuri kwa kutoa incentives kwa wawekezaji wetu. Lakini kubwa zaidi bado ziko changamoto. Changamoto kubwa tulionayo kwenye uwekezaji ni suala zima la ardhi. Wanakuja wawekezaji wanataka kuwekeza lakini kinacholeta kikwazo ni kwamba TIC hana ardhia ambayo anaweza akampa mwekezaji, na bahati mbaya mifumo hii hai-link. Wizara ya Ardhi na TIC bado hawakai pamoja. TIC anamleta mwekezaji anamwahidi kuja kuwekeza lakini ikija hapa inachukua miaka mingi kuweza kulipa fidia kwa wakulima wetu au kwa watu walioshikilia ardhi. Kwa hiyo jambo hili tuliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, zipo kampuni kubwa zenye uwezo wa kuzalisha hapa nchini katika baadhi ya maeneo ambayo ni nyeti, iwe katika eneo la vioo, glass na mambo mengine. Serikali inaweza kuongea nao, kwamba, je kama tukiwapa mtaji zaidi mnaweza mka-double production? Na tukaangalia, yapo maeneo tunaweza tukauza. Sisi katika nchi za SADC ni wazalishaji wakubwa katika maeneo mbalimbali. Masoko yetu tunayo; Congo ni soko letu kubwa. Tunafanyaje ili tuweze kuongeza uzalishaji na tuweze kupata fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, Serikali ilileta hapa Sheria ya Local Content lakini sheria hii haisimamiwi katika maeneo mbalimbali. Bado kuna material ya kwenye viwanda yanaagizwa kutoka nje ilhali katika nchi yetu yapo. Sasa kwa mfano kwenye cement tulikuwa tunatumia chuma ya hapa nchini. Imetokea gafla sasa viwanda vinaagiza clinker kutoka nje ya nchi. Mimi katika jimbo langu tulikuwa tunazalisha sana chuma ambayo tulikuwa tunatumia kwenye viwanda vya hapa nchini, sasa hatuzalishi halitoki hata lori moja. Sasa mambo kama haya tungeweza kuzuia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile yapo madini mbalimbali ambayo yanapatikana kwa wingi katika nchi yetu, bado nayo tumeruhusu viwanda vinaamua kuweza kuleta hapa nchini, jambo hili tuliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nimelesema sana kwenye suala zima la nyama. Dodoma sisi tuna kiwanda cha machinjio ya Kizota, na bahati mbaya sisi baadhi ya nchi zimetufungia tusipeleke nyama kwenye nchi zao kwa sababu ya machinjio yalivyokuwa na uchakavu. Vipo viwanda viwili, vitatu vya wawekezaji lakini havikidhi matakwa ya kupeleka nyama kwenye nchi hizo. Lakini kiwanda hiki cha Kizota kinahitaji bilioni mbili kuweza kukarabatiwa. Mimi huu ni mwaka wa tatu naongea na Serikali, hadi naona huruma kama ningekuwa na bilioni mbili ningeweza kutoa mimi mwenyewe kukarabati pale. Sasa miaka mitatu consecutively bilioni mbili hatuwezi kukarabati pale

Mheshimiwa Mwenyekiti, na tatizo lililopo ni kwamba mimi nimewahi kufanya biashara ya nyama; hakuna sehemu ambayo inategemewa kama central zone. Na viwanda vingine siwezi kusema ambavyo vya watu binafsi, ukianza kupeleka kwake kuuza baadaye anachukua lile soko. Kwa hiyo wafanyabiashara wetu wanapata shida vilevile hatupati faida ya mifugo. Mheshimiwa Waziri wa Fedha nakuomba sana bilioni mbili tuweze kukarabati kiwanda kile, nakuomba sana sana sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu wakandarasi wetu katika nchi yetu. Naishukuru sana Serikali imetoa kipaumbele kikubwa kwa wakandarasi nchini. Shida iliyoko ni kwamba wanachelewa kulipwa malipo yao, jambo hili Serikali iliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba, duniani kote mashirika ya bima (insurance) ndio yanayobeba riski katika biashara. Sasa siku hizi wakandarasi wetu wakienda kuchukua bima kwenye mashirika ya bima wanaambiwa watoe collateral. Sasa kwenye benki naambiwa nitoe collateral na kwenye shirika la bima nako naambiwa nitoe collateral; sasa kazi ya bima wanasema ni risk aging. Sasa bima nayo inataka nipeleke collateral. Na tunakoelekea kuna siku tutaona bima inatangaza kuuza nyumba ya mtu fulani ambacho duniani kote hicho hakipo. Sasa jambo hili kwetu unaambiwa kwamba lete collateral ili uweze kupata bima. Sasa risk anayoichukua mtu wa bima iko wapi? jambo hili naomba tuliangalie sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine tuna ushindani wa makampuni ya wakandarasi kutoka nje ya nchi. Wenzetu wanapewa mazingira mazuri, wana benki zao, lakini vilevile wana risk company zao ambazo ukilinganisha na kiasi ambacho tunawatoza wakandarasi wetu ni tofauti kubwa sana. Kwa maana hiyo unataka mimi nilyefungwa miguu wote tukimbie mita 100 ilhali mwenzangu hajafungwa miguu. Jambo hili kama tunataka kuinua wakandarasi wetu ni makusudi kabisa tufanye hivyo na kufanya hivyo kwamba fedha yetu itabaki hapa. Mheshimiwa Waziri naomba jambo hili tuliangalie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kazi ya Serikali duniani kote ni kuhudumia wananchi wake, iwe katika eneo la afya na katika maeneo mengine. Tuna tatizo. Wapo wahisani wanatusaidia katika maeneo ya afya na katika haswa suala zima la maji…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Malizia Mheshimiwa sekunde 30 muda wako umeisha.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimalizie; ni kwamba wahisani hawa wanavyoleta vifaa vya kuja kuleta miundombinu ya maji wanatozwa fedha kwa kodi na jambo hili linawavunja moyo. Kwangu nina mwisani ambaye ameleta takriban bilioni mbili ametoa kodi kama milioni 600, fedha ambayo ingeweza kutumika kujenga mradi mwingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru lakini nataka niseme kwamba Serikali iangalie namna ya kuweza kuondoa kodi kwa wahisani wanaoweza kutusaidia katika maeneo ya huduma za wananchi. Nakushukuru sana, ahsante sana.
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nafurahi kupata nafasi hii niweze kuchangia kuhusu Mpango huu uliowasilishwa na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu zaidi nataka nijikite kwenye suala zima la kilimo. Wachangiaji wengi wameonesha namna gani tunaweza kuendelea kwenye suala zima la kilimo. Ni dhahiri kwamba, nchi za Afrika tumekuwa tuna-export zaidi madini kwa maana ya extractive lakini tumekuwa hatufanyi vizuri katika ku-export mazao ya kilimo. Kwa hiyo, nataka nirudie na kusema kilimo tunahitaji wawekezaji lakini vilevile tunahitaji Serikali iwekeze kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu nataka nijikite zaidi kwa Mkoa wa Dodoma. Mkoa wa Dodoma unachukuliwa ni mkoa ambao hauwezi kustawisha mazao na kilimo kiko chini lakini tujiulize ni kiasi gani cha maji kinachopotea katika mkoa huu. Nianzie tu karibu pale Kibaigwa, lile bonde linavyotoa maji kwenda kule. Nenda Mpwapwa ile milima na mabonde yale, nenda hadi Mto Ruaha pale, anza kushuka njoo huku Dodoma, ingia Chalinze hapa uende hadi Bahi kule na swamps zote zile, lakini maji haya miaka nenda rudi yamekuwa yanapotea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewahi kwenda Egypt. Ukifika Egypt huwezi ukadhani kama uko kwenye jangwa. Egypt baadhi ya watu hawajawahi kuiona mvua maana mara nyingi inanyesha mara moja tena ni vinyunyu kwa mwaka na kama umelala huioni tena, lakini ni nchi ambayo it is very green kuanzia Cairo mpaka Alexandria, nchi yote imestawishwa kwa umwagiliaji. Naichukulia Dodoma iko sawasawa na Egypt na Israeli. Tena nazilinganisha tu basi lakini sisi hatuwezi kulinganishwa na Israel na Egypt, sisi tuko better off.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa takwimu za mwaka 2017, export value ya Egypt katika mazao ya kilimo ilikuwa ni Dola bilioni 2.2. Ukija Tanzania export ya mazao ya kilimo ilikuwa ni Dola 8,000,030 na hiyo siyo kwenye hotculture products ni mazao ya pamba, chai na kahawa. Kwa hiyo, nachotaka kusema ni kwamba tuna nafasi kubwa ya sisi kuweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Dodoma hapa tuna zao la zabibu lakini hatujalitendea haki. Nchi ya Israel imeweza ku-export ule mchuzi kwa thamani ya Dola milioni 240 kwa mwaka lakini zabibu ya Dodoma ndiyo zabibu ambayo unaweza kui-train izae muda wowote unavyotaka. Zabibu ya Dodoma wanasema ni nzuri katika dunia nzima kwa maana ya sukari lakini na namna ya ku-train kwamba iweze kuzaa. Unaenda hivyo hivyo Egypt, wenzetu wako mbali kwenye kuuza mchuzi wa zabibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye hoja yangu kwanini nataka kusema kwamba Serikali iwekeze kwenye kilimo. Tunahangaika kuchimba maji ya chini, tunatafuta maji underground huko kwenye miamba maji ambayo hatuyaoni ndiyo tunahangaika nayo, lakini maji yanayopita kila mwaka hapa mwaka huu yatapotea na mwakani yatapotea, hivi hatuwezi kweli tuka-tap maji haya yakutosha na tukaweza kulima kwa uhakika muda wote. Naamini kabisa Mkoa wa Dodoma huu unaweza hata ukalisha kwa kiasi kikubwa kulisha hata nchi yetu kwa maana ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna ardhi nzuri, ina rutuba lakini tunaenda hadi lini kwa utaratibu huu, maji yanapotea muda wote na nataka niseme wenzetu wamejikita zaidi kwenye hotculture ambayo kwanza hutakiwi kutumia maji mengi, ni maji yanaenda kwa utaratibu,acha hii massive kama tunavyomwagilia katika mazao mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo, nataka niishauri Serikali kwamba hebu tutoke kwenye kutafuta maji chini ya ardhi, tutumie maji haya ambayo tunayo kwenye mito.Wakati tuko Egypt nilikuwa kwenye delegation, mkuu wetu wa msafara aliulizwa kwanini Tanzania mna maji lakini bado hamfanyi vizuri kwenye kilimo. Tulienda kwenye shamba la ng’ombe 35,000 jangwani Egypt, kwanza yule mwenye shamba alihojiwa akaulizwa na Waziri wetu kwamba...

MWENYEKITI: Ng’ombe 35,000?

MHE. ERNEST K. NOLLO: Ndio ng’ombe 35,000.

MWENYEKITI: Kongwa Ranch ng’ombe hawafiki 10,000, endelea tu Mheshimiwa.

MHE. ERNEST K. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwahiyo shamba lile linalima nyasi kwa umwagiliaji jangwani na sera ya Egypt ni kwamba unaweza ukapata maji kwenye Mto Nile, lakini mtu wa Egypt anasema unatakiwa uchimbe kama hujayapata hujachimba. Kwahiyo mtu wa Egypt ataenda chini miles na mile lazima ayapate maji. Hii spiritna maji tuliyonayo hata Mwenyezi Mungu nataka niseme anatushangaa na atatushangaa kweli kweli.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka miujiza gani na maji haya tuliyonayo, ile pale nimetoa mfano pale Kibaigwa, kuna kipindi utadhani ni bahari, lakini maji yale yanapotea. Njoo kwetu Bahi sasa tuna-swamp ambayo imejaa maji kwelikweli, lakini hatuwazi kulima nyasi kwa kumwagilia, tupate maziwa yakutosha muda wote, hatuwazi maji yenyewe yatutosheleze, hatuwazi maji kwa ajili ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tungefanya hata anasa kama Kazakhstan, walichofanyawalihamia mji mpya ule wa Almaty, wakasema sasa tutengeneze kabahari, wakatengeneza bahari, maana waliona watu wengi wakiwa wana-relaxkama ilivyo Dar es Salaam wanaona bahari, ikaja kujengwa bahari, ni matumizi ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa uwekezaji kama wa umeme na reli ni gharama kubwa sana, lakini na hili nalo tulifanye, hivi kweli Serikali kwa maana tumetoa sasa ma- exavetor mwezi mzima wanachimba, hatuwezi kupata bwawa kubwa ambalo tutaweza kumwagilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikitoka hapo wenzangu wengi wamesema kwa habari ya mafuta,edible oil. Tumeongea sana, hivi ukatoa viwanda viwili tu pale Singida viwe vya bilioni 700, bilioni 500 tunamaliza kabisa habari ya edible oil kwenye nchi hii. Tuache habari ya kwamba tukuze michikichi baadaye tuanze kupata mafuta, lakini alizeti tukiamua miaka miwili hii tunamaliza habari yaku-import edible oil.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii,lakini kwa kweli nataka niseme Serikali jambo hili la uwekezaji kwenye kilimo tulichukulie serious, kwa maana ya kwamba hatuwezi kuwekeza kushindana kama alivyosema muwasilishaji alisema tunataka tuwe na ushindani wa kibiashara, lakini nashindana na nani katika sekta ipi? Sisi mashindano yetu yawe kwenye kilimo, tulikuwa na wenzenu akina Malaysia, akina Hongkong na akina Singapore, wale walikuwa ni wenzetu, lakini sasa wameshatoka kwenye uzalishaji wa kilimo wako kwenye teknolojia lakini sasa sisi tuko na wenzetu washindani kwenye sekta ya kilimo bado tuna lag behind, kwahiyo tunashindana vipi? Nataka niseme kwenye mambo elekezi seriouskwa maana ya kwamba sisi tuko kwenye stage ya uzalishaji kwenye teknolojia hatupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio kile ulichokuwa unasema kwamba ku-exportbrain, ile ni serviceindustryambayo sasa dunia ya wajanja na wameshafikia hapo tunawapataje akina Heron Max, tunawapataje hawa jamaa wa facebook,kile ndiyo kitu cha msingi sasa, unatengeneza kitu kidogo lakini unatoa bilions of money, sasa huko sisi hatujafika, lakini mambo mengine haya kwa mfano ya uwekezaji wa watu wetu, tunaweza tukafanya na tukaweza kupiga hatua kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. KENETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia katika Wizara hii ya Ujenzi. Nilitaka nichangie katika maeneo mawili. Kwanza nichangie kuhusu bandari yetu ya Dar es Salaam na vile vile nitachangia kuhusu suala zima la barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bandari yetu ya Dar es Salaam ni bandari inayohudumia nchi sita katika ukanda wetu huu, lakini bandari yetu hii imekuwa na changamoto nyingi kwa maana ya efficiency ya vitu vinavyokuja kuweza kutoka sasa kwenda kwenye nchi wanazotegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Benki ya Dunia, inasema nchi majirani wanaotumia Bandari ya Dar es Salaam, kwa ujumla wanapata hasara ya dola milioni 830 collectively kutokana na; niite ni uzembe unaotoka kwenye bandari yetu, kwa maana ya kuchelewa kwa muda wa vitu kutoka na hata urasimu usio wa lazima pamoja na udokozi unaofanyika bandarini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, World Bank wanasema bandari yetu ukilinganisha na bandari washindani katika ukanda wetu, ya kwetu inaonekana iko expensive kwa vigezo vyote hivyo. Vile vile wanasema Tanzania ikiamua kusimamia bandari yake, inaweza kuondoa loss ya shilingi almost bilioni 175 ambayo ni total loss kwenye economy pamoja na loss ya revenue tunazozikosa kwenye bandari yetu. Kwa hiyo, ninachotaka kusema kwa wenzetu wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, ipo haja kubwa sana ya kusimamia bandari yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia, sijui kuna kigugumizi cha nini? Tumeona nchi kama Singapore wanatumia bandari na viwanja vya ndege, wameendelea, sisi tunataka tupate miujiza ya aina gani? Pamekuwa na mizengwe mikubwa sana kwenye bandari yetu. Kwa hiyo, nataka Wizara hii na Mheshimiwa Waziri anasikiam hebu wakijite kwa ajili ya kuiboresha bandari yetu kwa kuondoa tu urasimu ambavyo ni vitu vya kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikija kwenye suala la barabara, Wizara hii imeonekana kufanya kazi nzuri kwa kutumia agency ya TANROADS, lakini hawapati fedha ya kutosha. Kwa miaka mitano mfululizo, bajeti hii haijaongezeka, lakini kazi walioifanya ni kubwa. Sasa tunategemea miujiza gani kama chombo hiki kinachotusaidia kwa kuunganisha nchi yetu katika barabara, lakini bado wanapata fedha kidogo? Kwa hiyo, hili tuliangalie, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi iongezewe fedha za kutosha na hata bajeti yenyewe basi iweze kutekelezwa kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, alipokuwa kwenye kampeni pale Manyoni, aliahidi kutengeneza barabara kwa kiwango cha lami kutoka Manyoni kuja Itigi - Heka - Sanza - Chali kwenye Jimbo langu la Bahi Kijiji cha Chali; na barabara hii ni muhimu sana, maana yake ukija Halmashauri ya Manyoni na Bahi, tunaitegemea sana kwa maana ya shughuli za kiuchumi katika Mji huu wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, barabara hii ikitengenezwa kwa kiwango cha lami kama nilivyotaja, kuanzia Manyoni - Itigi - Heka kuja - Chali Igongo - Chali Makulu - Chali Isanga, unakuja unatokezea Chipanga unakuja Mpalanga – Bihawana, utakuwa umetengeneza link kubwa sana ambayo itachochea uchumi katika Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo mengi barabara zimeonyeshwa, lakini kuna vitu vingine ambavyo ukiangalia huwezi ukaelewa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)


MHE. KENETH E. NOLLO: Naunga Mkono hoja Ahsante sana.


Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Wizara hii ya Kilimo ambayo ndiyo Wizara mama na ni tegemeo katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwanza mimi niseme kwa masikitiko makubwa matarajio niliyokuwa natarajia bajeti hii kutoka kwa Profesa Mkenda si kwa kiwango hiki ilivyokuja.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na matarajio makubwa sana, nilijua Wizara hii bajeti yake itakuwa na transformation lakini ukiiangalia na bajeti zilizopita it is all most the same. Sioni picha kubwa ambayo nilikuwa nayo ya Profesa Mkenda. Kwa kweli bajeti hii binafsi sijaridhika kutokana na nilivyokuwa na matarajio makubwa kutoka Profesa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bajeti hii kwenye miradi ya maendeleo imetengwa shilingi bilioni 150 ukiacha matumizi mengine. Hivi kweli kilimo cha nchi hii unakipangia bilioni 150 Tanzanian shillings, kwa kweli hatuendi mbele.

Mheshimiwa Spika, nikija Kanda ya Kati kupitia kwenye bajeti huoni strategic vision kwamba hapa Kanda ya Kati kilimo kinakuja kuwekwa sawasawa, huoni programme, huoni chochote. Ukiisoma bajeti imegusagusa tu kwa kudonyoadonyoa na ni story kwamba hapa tulifanya hivi na pale tulifanya vile, lakini picha hasa kubwa ya Wizara ya Kilimo tunaelekea wapi huioni kwenye bajeti.

Mheshimiwa Spika, mimi nataka niseme na nashauri Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri tukimaliza bajeti hii hebu waende nje; Waziri aende Egypt lakini Naibu Waziri aende Zimbabwe. Zimbabwe wamenyang’anya mashamba kutoka kwa Wazungu na dunia nzima ikajua sasa Zimbabwe inaenda kufeli lakini wamefanya mapinduzi makubwa sasa kwenye kilimo, kwetu hapa hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu hailimi, tuko strategically positioned kwa ajili ya kuilisha Middle East na Uarabuni…

SPIKA: Mheshimiwa Waziri wa Maji unakatiza kati ya mzungumzaji na Kiti lakini pia nilishazuia watu kumfuata Waziri Mkuu, ulikuwa haupo ndiyo maana, endelea Mheshimiwa.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, sisi tumekaa katika position nzuri ya kuilisha Middle East na nchi za Kiarabu ambazo wenzetu kule ni jangwani, lakini ukienda kwenye masoko ya Doha na Abu Dhabi vitu vyote vinatoka South America hadi ndizi na mchicha sasa hii nchi tunaenda huko lini? Ukiwa kwenye ndege unatua hata tu barabarani unakwenda Arusha unakwenda wapi hakuna plantation zozote katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, matreka yanayoingia hapa huwezi kulinganisha na Zimbabwe ambao Waafrika wenzetu wameingiza. Kwa hiyo, mimi nachoona bado tunapiga mark time, ASDP I&II zilifadhiliwa sana na donner partners walivyojitoa kwenye basket fund ile ya kusaidia kilimo sasa hivi hakuna ni story tu, ASDP II haina kitu.

Mheshimiwa Spika, nadhani kwenye kilimo tuwe serious, aligusia Mheshimiwa Kandege hapa hakuna kitu ndugu zangu tuseme ukweli kama tunataka kweli twende kwenye kilimo hatujaamua ndugu zangu. Wenzangu wameongelea Minjingu na maeneo mengi hatufanyi vizuri. Sasa nchi hii tunataka kuendelea, lakini tunaendeleaje kilimo tunakipuuzia? Kwa kweli nataka niseme bajeti hii imekuja chini ya kiwango hai-reflect hasa tunataka twende wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nchi yetu kama nilivyosema tumejaaliwa tunalima sana mahindi na nchi zinazotuzunguka wanatutegemea sisi lakini bado hatujakaa sawasawa. Hatuwezi kulisha South Sudan, kuna watu tu wametu-block hapo karibu basi hatuwezi kwenda South Sudan. Congo walikuja wanataka…

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa taarifa.

SPIKA: Ndiyo, Mheshimiwa Naibu Waziri tafadhali.

NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mchangiaji rafiki yangu Nollo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, pamoja na nia njema sana ya maelezo yake juu ya mchango wa sekta ya kilimo, naomba nimpe comfort kidogo, najua baadaye Mheshimiwa Waziri ataeleza, lakini katika bajeti hii ya mwaka 2021/2022 ASDP II kupitia mradi utakaofadhiliwa na IFAD, Wizara ya Kilimo (mazao na mifugo na uvuvi) tutapata zaidi ya shilingi bilioni 150. Pesa hizi zitakwenda moja kwa moja katika vikundi kusaidia mambo ya mbegu na mengineyo. Kwa upande wa mifugo huko tutakapofika katika Wizara yangu pia vilevile itaonekana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimpe comfort na ikimpendeza baadaye nafikiri kupitia Mheshimiwa Waziri atamuonyesha kwa undani zaidi.

SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa Nolla unapokea taarifa hiyo?

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, siipokei taarifa hiyo kwa sababu hatujapata hizo fedha kutoka IFAD, tunaanza kujadili kwamba tukiokota fedha tugawane, sasa ni story hiyo.

MBUNGE FULANI: Maoteo.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Hatuwezi kujadiliana maoteo. Mheshimiwa Spika, kwa kweli nachotaka kusema Serikali iwe serious kwenye kilimo kwani bado hatujawa serious. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye Jimbo langu la Bahi tuna skimu za mpunga za umwagiliaji, hazijafanyiwa ukarabati muda mrefu. Mara ya mwisho zimefanyiwa ukarabati mwaka 1998. Skimu ya Ntitaa mwaka 2004 IFAD walitujengea ilifanya kazi mwaka mmoja lile tuta likavunjwa mabilioni ya shilingi hatujawahi tena kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nachotaka kusema hebu tuichukulie Wizara hii kama MSD inavyofanya kazi. Kilimo kikianza kufanya kazi kama MSD tutaendelea. Tuchukulie kwamba huu ni uhai wa nchi. MSD inaleta dawa na ndiyo maana tunaendelea kuwa na afya, lakini kwenye kilimo bado tunacheza.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Mambo ya Nje. Nchi yetu imekuwa inaheshimika katika sura ya kimataifa kwa muda mrefu sana. Lakini heshima ambayo tumekuwa nayo tangu enzi ya awamu ya kwanza ni kutokana na nchi yetu kuwa na misimamo thabiti katika kutetea haki na unyanyasaji wa aina yoyote katika nchi mbalimbali hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatukujipambanua tu kwa kutetea haki kwa kutetea waafrika wenzetu wanavyosanyanyaswa au kuonewa lakini tumeenda nje kabisa ya Afrika na kutetea kokote duniani ambako tunaona haki inabinywa. Nataka niseme hili kwa kuangalia kwamba nchi yetu sawa inaingia kwenye uchumi wa dipomasia, lakini tunafika mahali sasa tunaanza kwenda kama watu wanaotaka kujiuza, tunapoteza heshima yetu, tunapoteza sisi tusema maskini ambaye sasa hana aibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana sasa unaweza ukawa maskini, lakini aibu unayo, una heshima yako unalinda heshima yako. Nalisema hili kwa sababu moja, wiki mbili zilizopita dunia nzima imeona namna Palestina ilivyoshambuliwa kwa kiasi kikubwa ambacho binadamu yeyote hawezi akasema hiki ni kitu gani kinatokea. Nchi yetu hatujatoa hata tamko la kulaani, hata kusikitika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na mwingine anaweza aka-justify akasema mbona nao Hamas walikuwa wanarusharusha mawe upande ule, lakini ukiangalia kulichofanyika pale nchi yetu tulitakiwa tuweze kufanya condemnation kwa namna gani Palestina walivyofanyiwa. Hata Mwalimu alikuwa na msimamo thabiti kuhusu Palestina na msimamo wa nchi yetu ilikuwa ni kwamba pale inatakiwa mataifa mawili na juzi Rais wa Amerika huyu mpya amesema pale panatakiwa mataifa mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nataka nisema ni kwa nini tunaanza kupoteana, Waziri atuambie msimamo wetu kuhusu Palestina ni nini? Anachofanyiwa Palestina sisi msimamo wetu Tanzania ni nini? Hili Waziri atuambie na ikiwezekana basi leo alaumu kilichotokea juzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na msimamo mkali kuhusu Morocco, alijitangazia kwa west sahara anaitawala na sisi Tanzania tukawa wakali hata tukatoa influence yetu kwenye Umoja wa Afrika na Morocco akajaribu kuingia pale akazuiwa, lakini hili nalo tumepoteana kwanza tumefungua ubalozi wetu Algeria ambao ulikuwepo, lakini tume-extend na Morocco sasa tuna ubalozi ambao tunautumia ule wa Algeria. Lakini na hili nalo Waziri atuambie msimamo wetu kuhusu West Sahara ni nini? Tumekubali kwamba tunakuja kujengewa kiwanja basi imekuwa give and take tunawaacha West Sahara ambako ulikuwa msimamo wetu tangu awali. Hili nalo Mheshimiwa Waziri atuambie msimamo wetu kuhusu West Sahara ni nini sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kuhusu economic diplomacy ambayo wengi wameisema kwamba sisi tuangalie nchi yetu tunapata nini, ndio maana nikasema sasa ile ni maskini anayejirahisisha na nchi yetu imekuwa na heshima kubwa na watangulizi wetu walitumia damu na nguvu zote kutetea hili, lakini hatuwezi tukatumia kitendo cha uchumi wa diplomasia tuweze sasa kusema hili sisi walau kwa vile tunapata pesa basi hili tuliruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, balozi zetu tunazifungua, lakini ni lazima tuangalie kwamba tunapata nini pale. Economic diplomacy isichukuliwe kwamba sasa tumekubali ubeberu ututawale tunavyotaka na vyovyote itakavyoenda lakini lazima tuseme hapana kwa imperialism, ni nchi yetu lazima iseme bado kuna shida ya ubeberu na ubeberu wa namna yoyote ile nchi yetu lazima isema hapana, tusipoangalia tutakuwa ma-purpet wa mabeberu na tutasema kila kitu tutakabiliana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme hili kwa sababu moja wakati corona inaingia nchi yetu watu waliishangaa na tulionekana hatufai kwa nini atufungii watu wetu ndani, na hili tulisimama kidete, lakini majirani zetu na Afrika wakaanza kuwaambia sasa chukueni package ya kujinusuru na ya kunusuru uchumi wenu na majirani zetu wamekopa IFM, World Bank, nani hela nyingi sana, lakini sisi msimamo wetu tulisema kwamba kwenye hili hapana kama wanataka kutusaidia basi watupunguzie riba ya madeni haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na ninataka niseme na wizara waelewe tunakoelekea tunajipeleka kwenye chanjo, sawa, lakini kwenye jambo hili tuangalie tuwe na msimamo thabiti kwamba chanjo ile bado inazungumzwa kwa tofauti. Mheshimiwa Rais ameunda Kamati na imeshauri lakini ni lazima ndugu zangu wa Tanzania tuendelee kuliangalia hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bado twendeni kwa kushtukastuka, tusiingize miguu yote, kama tulivyostuka hatua za awali za kufungia watu wetu bado na hili lazima twende kwa kustukastuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu balozi zetu kama nilivyogusia tusipekele tu watu ambao wamesoma international relations, tupeleke watu mbalimbali wenye ujuzi, wataalam wa masoko, biashara, wa uwekezaji, lakini kwamba balozi anakuwa na afisa mmoja tu pale halafu mnategemea mpate chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unateuwa balozi kwenda Lubumbashi unamchukulia kwa minajili kwenda kusuluhisha tu migogoro, lakini bado tunanaangalia kwamba balozi wetu huyu atuletee nini Tanzania. Kinachotushinda ni kwamba tunashindwa sasa kuangalia potential zilizopo za kibiashara tuweze kuzileta hapa kwetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nilitaka nishauri, nchi yetu inavutia wawekezaji lakini tutaweza kupata wawekezaji wengi, lakini baadae tunaweza tukasema hawa watu wamekuja kutuibia kwa sababu moja tu, ukienda Malaysia kwamba mwekezaji lazima awe na mzawa, hapa kwetu tunasema lakini hatulifanyi, hata mzawa akiwepo anakuwa na ka-minor share na anakuwa diluted. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili tuliwekee mkazo kwamba ni lazima Mtanzania awepo kwenye kampuni ile na ashiriki kikamilifu, lakini kingine tuzalishe na sisi matajiri wa kwenda kuwekeza nje, Dangote yupo kwetu hapa ametengenezwa, lakini mkakati wa kumpeleka Bakhresa nje upo wapi, matajiri wetu mkakati wao huko wapi? Nataka nishauri kwamba Wizara ya Fedha na ninachukulia mfano wa nchi ya Ufaransa ina department ya Private Sector for Overseas Investiment na sisi tuwe na hicho na kitengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zetu wa China wakija hapa wawekezaji wao wanakopa hela kwenye Exim Bank ya China ndio maana inakuwa rahisi kuwekeza hapa kwetu. Sasa na sisi ni lazima tuwe na Overseas Department kwa ajili ya private sector ambayo itaweza kuwatafutia masoko, oppotunities na hata kuangalia namna gani Serikali iweze kufanya business negotiations badala kuwaacha waende namna hiyo walivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukifanya hivi tutasaidia nchi yet una kwa maana hiyo tutakuwa washindani katika biashara, katika shughuli za uwekezaji zinazofanyika na namna hiyo tutaweza kweli kusema tunatekeleza economic diplomacy.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nashukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nianze kwa kuipongeza na kuishukuru Serikali kwa utaratibu iliyochukua wa kutoa fedha shilingi 500,000,000 kwa kila jimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu huu nauona una tija zaidi tofauti na ilivyozoeleka. Kwa upande wa Jimbo langu la Bahi, shilingi 500,000,000 hizi zimenisaidia kutatua changamoto kubwa ya barabara inayotoka kwenye Kata ya Chifutuka ambayo iko kilometa 90 kutoka kwenye Makao Makuu ya Wilaya na wakati mwingine imekuwa inajifunga haipiti. Lakini kwa 500,000,000 hizi tulizozipata tunaenda kutatua kwa kiasi kikubwa tatizo hili la barabara na hatimaye kuweza kuleta maendeleo ya wananchi kupitia kata ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nataka niipongeze sana Serikali. Bajeti hii ina ahueni kubwa katika kuleta maendeleo lakini pamoja na hilo, tunakuja kwenye matumizi ya bajeti. Bajeti yetu imekuwa mara nyingi haifiki asilimia 70 katika matumizi hususan katika miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hasa Wizara wa Fedha aelewe na atambue hili kwamba bajeti yetu iwe ni rural centered development. Iangalie zaidi katika kutatua shida zaidi za wananchi waliopo vijijini na kwa kweli tuna shida kubwa sana vijijini. Tuna shida ya zahanati, kwa mfano Jimbo langu la Bahi sina zahanati 16, sina ambulance, hata ambulance zinazokuja ugawaji wake bado haueleweki. Ukigawanywa kama hivi tulivyopewa 500, 500 italeta ahueni. Kwa hiyo, nadhani hii model iliyotumika ya 500,000,000 tuiangalie katika bajeti iweze kutumika katika maeneo mengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya bajeti kupitishwa imekuwa tunasubiria kudra za Hazina ndiyo ziweze kutupatia katika maeneo yetu. Wakati mwingine unasikia upande fulani wamepewa, huku kwako hujapewa, kigezo hakieleweki. Ili twende sawa sawa, kuwe na equal distribution, ni lazima tuone namna gani. Kama tunaamua kutoa milioni 600 kwa ajili ya kumalizia maboma kwenye majimbo yote, ziende kote. Namna hii tunaweza tukaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niishie pale kwenye conclusion ya Waziri wa fedha kuhusu kadi ya njano na kadi nyekundu. Maneno yale yana busara kubwa ya kuonesha namna gani kiongozi wetu wa Taifa hili alivyosheheni uzoefu wa kuweza kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hivyo tu ni kwamba Mheshimiwa Samia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi. Chama hiki kina utajiri wa rejea katika uongozi. Ni chama ambacho kimepita katika vipindi vingi tangu kuanza mapambano ya uhuru lakini baada ya nchi yetu kupata uhuru. Lakini, hata hivyo vile vile kupambana na mifumo mbalimbali ili kujiletea maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Chama chetu cha Mapinduzi kimekuwa kinafanya reform kila wakati. Iwe katika kipindi kile sasa tunaanza kuimarisha viwanda Watanzania tuweze kujitegemea. Lakini hata hivyo, tuwe tumekuwa tunaangalia tunaenda na sera gani, tunajibadilisha kila mara kutokana na matakwa ya jamii yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliwahi kutoa Sera za CCM katika miaka ya 90. Lengo letu lilikuwa ni namna gani sasa tunaanza kwenda katika mageuzi ambayo yanatokea katika Dunia na sisi tuweze kuendana na namna Dunia inavyoenda. Kwa hiyo, nataka niwahakikishie Watanzania, Mheshimiwa Samia anarejea kubwa ya uongozi na ninataka niwaambie hakuna shaka ya kuwa na wasiwasi kwamba Mheshimiwa Samia hatalivusha Taifa hili. Atafanya vizuri zaidi kwa sababu ana msingi mkubwa ambao msingi umetengenezwa na Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, imetokea kasumba ya baadhi ya Mwenyekiti wa chama kimoja kuonesha kwamba kama ana kauli ya kuweza kulazimisha kila anachotaka yeye. Nataka tu niseme kama nilivyosema Samia ni Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi. Mwenyekiti huyu ambaye kidogo anataka kujipa ahueni kwamba eti anataka kuja 25 ashike dola alianza tangu enzi za Mzee Mkapa, Mzee Mkapa akaondoka yeye bado ni Mwenyekiti, akaja Mzee Kikwete yeye bado Mwenyekiti, amekuja Hayati Magufuli yeye bado Mwenyekiti. Sasa mtu ambaye amekosa pumzi kabisa amechoka hoi bina taaban anataka kuja kupambana na Mwenyekiti ambaye ni mpya kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia Mwenyekiti wetu ni Mwenyekiti ambaye ameonesha, Rais wetu ameonesha ni mtu anayejua hata Dunia inavyoenda. Ninyi mmeshuhudia hata mitazamo yake, juzi amesema kwamba sasa Taifa letu liangalie kuna mageuzi makubwa sana ya kidijitali yanatokea. Sasa hatuwezi kubabaishwa na Mwenyekiti huyu ambaye ni Mwenyekiti wa enzi na enzi, amekosa mvuto, amepauka na anajinasibu anasema wao ni makamanda. Kwanza nataka niwaambie, sisi tulikomboa nchi nyingi za Afrika katika kupigania uhuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wameanza kuvaa makombati hayo wanayoyavaa sisi tunawaona. Sisi tulishapigania uhuru na chama chetu kina heshima kubwa katika Bara la Afrika na ninataka niseme Mheshimiwa Samia sio wa kufanyiwa mashinikizo, yuko kwenye chama imara, anajiamini na nataka niseme tunaendelea kusonga mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika wa Kuzuia na Kupambana na Ugaidi ya Mwaka 2004
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue nafasi hii kwa dhati niipongeze Serikali kwa kuja na Azimio la Kuridhia Itifaki ya Mkataba wa Kupambana na Ugaidi. Zaidi jambo hili linatoka kwa pendekezo na muktadha kutoka Umoja wa Mataifa kwamba nchi katika Kanda mbalimbali na dunia kwa pamoja tuweze kushirikiana kupambana na ugaidi. Bahati mbaya, dhima na dhana hasa ya ugaidi bado inatofautiana kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. Vilevile bado kuna ulegevu mkubwa wa Umoja wa Mataifa wenyewe kutoa definition kamili ya nini maana ya ugaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ugaidi umekuwa unafadhiliwa na baadhi ya mataifa makubwa waziwazi na UN ipo. Ugaidi umekuwa kama unataka kuua mbwa mpe jina baya, baadhi ya nchi zimejaribu kutengeneza ugaidi kwenda kudhuru nchi zingine. Siwezi kuzitaja nchi hizo lakini ipo sponsored terror groups na jambo hili linatokana na mtofautiano wa kiitikadi kwamba huyu ni gaidi, kwa hiyo anaweza kuwa gaidi kwa mtizamo wa mwenzangu lakini kwangu vilevile asiwe gaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona katika historia wakati wa mapambano ya Kusini mwa Afrika, kikundi cha Nelson Mandela na Wapigania Uhuru wote wa South Africa waliitwa magaidi. Jambo hili bado linaendelea hata duniani, Mwalimu Nyerere alikwenda ziara Iraq mwaka 1979, wakati wanatoa ile inaitwa International Communiqué sasa maazimio ya pamoja na Iraq; Rais Sadam Hussein akataka waweke na kipengele kwamba kwa pamoja wamekubaliana kupinga uonevu unaofanyika kwa Wamarekani Weusi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwalimu Nyerere alikataa akasema we don’t subscribe to that conflict; japo kuwa sisi ni PAN Africanism. Kwa hiyo na sisi tunapoingia katika muktadha huu wa kupambana na ugaidi lazima kuwa na maeneo tusi-subscribe; lazima tuseme sawa lakini hili bado haturidhii kama ule ni ugaidi. Tukienda hivyo, tutaondoa ile dhana ya sisi kutumiwa, kwa maana ya kwamba mataifa makubwa na mengine yanayotufadhili katika mambo mbalimbali yanaweza yakatumia mwanya huu sisi kuingizwa kwenye migogoro ambayo haituhusu na kwa sababu tumeingia katika Itifaki hii, basi tutaonekana kwamba na sisi tuweze kuwa pamoja katika migogoro ambayo wanayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzangu wamesema kwa maana ya kanzidata ambayo ipo Algeria kwenye security na kwa maana ya ku-share information ni jambo la msingi; lakini siyo kila information utataka uitumie. Kwa hiyo, naiomba Serikali katika jambo hilo kwamba ni lazima tuseme kuna maeneo tunakubaliana kwamba huu ni ugaidi na kuna maeneo mengine lazima tukatae tuseme huu siyo ugaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashindwa kutaja baadhi ya nchi na baadhi ya vikundi, lakini jambo hili linaendelea. Ukienda nchi kama Qatar kuna vikundi vipo pale lakini nchi zingine wanasema wale ni magaidi; lakini wamewa-host wanakaa pale. Ukienda Palestine inachukuliwa ni magaidi, lakini kuna nchi hata sisi wenyewe tunasema Wapalestine siyo magaidi. Kwa hiyo, muktadha huu usitupeleke moja kwa moja katika Azimio hili, sasa katika context ya Afrika na sisi hata Kikanda bado kuna maeneo tunakubaliana hatukubaliani. Serikali zetu lazima tuchukue wajibu kwamba tusitumie mabavu ya Serikali kunyanyasa vikundi vingine na tukavipa nembo ya ugaidi. Jambo hili katika SADC na Afrika kwa ujumla ni lazima tuliangalie, kupitia hili Azimio tuwe na model nzuri ya kusema ugaidi ni nini na namna gani tuna-combat nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwetu hapa yalitokea pale Rufiji ilikuwa ni ugaidi, lakini tumeona Msumbiji imekuwa ni ugaidi, wenzetu wa West Africa wanasumbuliwa sasa na ugaidi nchi karibu tatu zote zile. Kwa hiyo, ninachotaka kusema ni kwamba lengo letu tuwe katika nyanja zaidi ya kiusalama badala ya kushabikia ugaidi hasa kwa maana ya context ya dunia ambapo bado hatujakubaliana gaidi ni nani katika mtazamo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nchi zetu na Serikali zetu ni lazima ziangalie mipasuko katika jamii kwa kuwapelekea rasilimali, mgawanyo wa rasilimali uwe unakwenda sawasawa; moja ya maeneo yanayozalisha ugaidi ni baadhi ya jamii kutengwa, ni baadhi ya jamii kuona sasa hawafaidiki. Vilevile nchi zetu zina utajiri wa madini, baadhi ya maeneo ugawaji wa rasilimali haujakaa sawasawa; kwa hiyo, Tanzania kama kioo na kama kiranja wa ugawaji sawa wa rasilimali, ni lazima tuzikumbushe nchi zingine za Afrika ambazo tunaingia nazo katika Itifaki hii kwamba, lazima kuwe na usawa wa kugawanya rasilimali ili kuondoa minong’ono katika vikundi vingine katika jamii na hasa kuzalisha ugaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, ni lazima sote tukubaliane kwamba mitazamo ya kidini imetumika katika ugaidi na kwa bahati mbaya yapo maeneo ambayo wamepata indoctrination hasa katika watoto wadogo na baadaye kuingia katika stage kubwa ya ugaidi. Pamoja na hilo lazima na Tanzania iendelee kuwa mfano katika hizi nchi nyingine za Afrika kwamba sisi tumewezaje kukaa na dini mbalimbali, tumewezaje kuishi pamoja na tumewezaje kuvumiliana katika kuwa makabila zaidi ya 127. Kwa hiyo, tunavyoingia kwenye Itifaki hii tuna kazi ya kuwaonesha wenzetu, tuna kazi vilevile ya kutoa somo kwamba ni namna gani katika jamii nyingi kwa ujumla na namna gani una in grace zile differences ili uweze kuwa na jamii ambayo haina mikwaruzano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukifanya hivyo kama nilivyosema pamoja na kuingia katika itifaki hii sisi tuwe kiranja katika kuonesha wenzetu ni namna gani wanaweza wakakumbatia zile tofauti zilizopo, tumefanya hivyo katika miaka mingi, tumekuwa wasuluhishi migogoro ya Maziwa Makuu. Kwa hiyo, kama nilivyosema tuna jukumu kubwa lakini kikubwa zaidi tusitumie ugaidi katika context ambayo baadhi wanazo tofauti zao za kisiasa na baadhi ya vikundi vinafadhiliwa na Serikali za nchi mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikushukuru na mimi kwa kunipa nafasi hii niweze kuchangia katika Wizara hii ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nifanye rejea kwamba duniani kote na tukiangalia tangu kuanza kwa shughuli ya viwanda duniani katika historia imekuwa inahusishwa na sera ya mambo ya nje, wakati Japan kupitia Waziri wake wa Viwanda na Biashara, na wakati ule kipindi kile cha Marekani zaidi walikuwa wanaangalia Rais anayekuja ana mtizamo gani na katika siasa ya sasa ya mambo ya nje wanaangalia Rais anayekuja ana mtizamo gani na hiyo ina reflect biashara ya nchi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu katika vipindi mbalimbali tumekuwa na marais wetu katika Awamu ya Kwanza mpaka sasa Awamu ya Sita, sote tunajua sera ya Mwalimu Nyerere kuhusu foreign policy na suala la viwanda, tukija hivi karibuni katika Awamu ya Mheshimiwa Kikwete, Rais Kikwete katika historia ya nchi yetu ndiye Rais aliyeenda zaidi katika kujiunganisha na mataifa ya nje katika suala zima la biashara na wazungu wanasema kama alienda ku-strike deal, ali-strike deal nyingi lakini bahati mbaya utekelezaji wake haukuweza kwenda sawasawa na matamanio ya Rais Kikwete mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumempata Rais Magufuli yeye sera yake zaidi ilikuwa ni ya protectionism, si zaidi ya nje, lakini alitaka kukuza base ndani ya nchi. Tumempata Mheshimiwa Samia katika Awamu ya Sita yeye zaidi anaangalia foreign policy na anaangalia zaidi katika kutafuta mitaji ya nje katika kukuza biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi kifupi tumeona Mheshimiwa Samia ameenda katika nchi za Ulaya, ameenda Amerika, ameenda na Uarabuni. Safari ya Ulaya peke yake ina mikataba kiasi cha trilioni 11.7; lakini ile ni mikataba na katika mikataba kuna makubaliano, kinachosumbua katika nchi yetu ni namna gani sasa kufuatilia mikataba ile na kwa dhati mimi nataka nimpongeze sana Rais wa Awamu ya Sita anapokuwa nje mazungumzo yake mengi ni biashara na siyo misaada. Ukimnukuu na ukimfuatilia Rais wetu hayuko katika syndrome ya misaada anaangalia zaidi biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wasiwasi wangu ambao naupata kwamba tutapata mikataba mingi, lakini umadhubuti wa kutekeleza mikataba ndiyo changamoto tuliyonayo katika nchi yetu. Mikataba itakuja mingi na Rais atasafiri, lakini nani anafuatilia kutekeleza mikataba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo tatizo na Mheshimiwa Rais amekuwa anarudia kwamba kuna tatizo la coordination ndani ya Serikali na hili ni kweli ukiangalia katika Wizara hizi za biashara kwa maana ya Madini, Kilimo, Utalii na Uwekezaji, Viwanda na Biashara lakini nani anawaunganisha, hakuna chombo kinachowaunganisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulikuwa na Presidential Delivery Unit, wenzetu wa Malaysia wanaendelea nayo na ile ndiyo unaweza ku-coordinate, watu wa Wizara wakishatoka nje na ziara na Mheshimiwa Rais wakifika documents zinawekwa inakuja ziara nyingine documents zinawekwa lakini ni nani anasema sasa mkataba ule wa Belgium mkataba ule wa Ufaransa ni nani anafanya sasa jambo lifanyike. (Makofi)

Kwa hiyo, tutaenda sana nje, Rais wetu atafanya sana mahusiano ya mikataba, lakini utekelezaji ni changamoto. Kipindi cha Rais Kikwete tuliwahi kufanya makubaliano ya kwamba wale IBM ile the brain behind ya computer waje hapa Tanzania, lakini mikataba ile ilipotea, hatukuweza kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende haraka haraka tunaishauri Serikali kwanza iweke kitengo cha uwekezaji kwa mitaji ya nje na mitaji ya ndani, tunavutia wawekezaji waje ndani, lakini tuna Watanzania ambao wana uwezo mkubwa hatujaweza kuwaendeleza. Naishauri Serikali tuna makampuni makubwa wakina Azam, benki zetu kubwa kama CRDB sasa wako Burundi, je, tuna mpango gani wa kupanua zaidi kwamba na sisi watu wetu tuweze kuwatafutia maeneo na mitaji zaidi na masoko kwa ajili ya kwenda kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaweza tukataka kwamba tulete mitaji ndani, lakini mitaji tuliyonayo hatujaiendeleza, tunao Watanzania wenye mitaji kuanzia shilingi bilioni 10 kwa nini Mheshimiwa Rais asikutane nao na tuweze kupanga namna gani tunaweza kuwasaidia ili waweze kufanya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Dangote tunayemuona leo ametengenezwa na Serikali ya Rais Obasanjo, Dangote alikuwa mchuuzi wa kawaida lakini akatengenezwa na Rais Obasanjo, sasa na sisi ni lazima tufanye hivyo tuwatengeneze matajiri wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa lipo suala la kupanda bei vitu, nataka niseme kwenye eneo moja tu na Mheshimiwa Waziri wa Viwanda anielewe. Nchi yetu kila inavyofika Disemba cement inapanda katika kipindi cha miaka mitatu minne iliyopita na tatizo lililopo ni kwamba muwekezaji mkubwa wa cement anazima kiwanda kila mwezi wa 11 afanye matengenezo. Cement ilikuwa shilingi 16,000 mwezi Novemba alipozima ikapanda ikaenda hadi shilingi 20,000 na inaendelea hivyo hivyo. Sasa na ninaamini na mwezi wa 11 mwaka huu tena atazima kiwanda na cement itapanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa nini mchezo huu tuendelee kuwa nao ambao tunawaambia Fair Competition waangalie wadhibiti lakini hawawezi kufanya hivyo, ni kwamba kinachotokea ni kwamba ni mtu mmoja anazima kiwanda kwa ajili ya matengenezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Azimio la Bunge la kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuimarisha demokrasia nchini na kukuza diplomasia ya uchumi
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia katika hoja hii ya kihistoria.

Mheshimiwa Spika, kiongozi yeyote duniani hupimwa kwa nyakati na mazingira ambayo anachukua nchi katika kuiongoza. Mazingira aliyoyachukua Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Katika kuiongoza nchi hii, yalikuwa ni mazingira magumu, yalikuwa ni mazingira ya kipindi cha giza, yalikuwa ni mazingira ambayo kila mmoja wetu katika nchi hii alikuwa hajui ni wapi tunaelekea.

Mheshimiwa Spika, katika historia ya nchi yetu hajawahi kutokea Rais aliyepo madarakani akafariki akiwa madarakani. Vile vile, katika nchi yetu ilikuwa ni wakati mgumu kwamba sasa tunakwenda katika mlengo upi? Mazingira aliyotoka nayo Mwalimu Nyerere wakati anaichukua nchi hii yalikuwa tofauti, Mzee Mwinyi hivyo hivyo, Mzee Mkapa hivyo hivyo, Mzee Kikwete hivyo hivyo, Mzee Magufuli ilikuwa tofauti na Mheshimiwa Samia ikawa tofauti vile vile.

Mheshimiwa Spika, uhodari wa Rais Samia unaonekana katika maeneo haya. Kama nilivyosema alichukua nchi wakati tukiwa katika majonzi, vile vile alichukua na kuongoza nchi hii akitoka katika Chama kikubwa ambacho ilikuwa ni kazi ngumu kukiunganisha. Ninyi mnafahamu duniani kote anapotoka Rais madarakani kunakuwa na mipasuko mikubwa, yanatengenezwa mazimwi kumtisha Rais aliyeko madarakani, zinatengenezwa hoja za kusema wale ni wa kwako na wale sio wa kwako, zinatengenezwa hoja kwamba wale ni bora na wale sio bora. Hata hivyo, vikwazo hivi Mheshimiwa Samia alivuka ndani ya Chama cha Mapinduzi na Chama hiki imekuwa imara.

Mheshimiwa Spika, hapa leo tunaposema, huwezi ukatanabaisha kwamba wale wa Rais Samia, wale sio wa Rais Samia, wale wa Chama cha Mapinduzi bora, wale sio wa Chama cha Mapinduzi bora, wote sisi tumekuwa chombo kimoja kwa sababu ya uthubutu wa Rais Samia.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo sote tutakubaliana wakati Mheshimiwa Samia anachukua madaraka nchi yetu tulikuwa tumehasimiana sana kisiasa kwa tabia zetu, kwa namna tulivyotoka. Mheshimiwa Samia amechukua uongozi wa nchi hii kukiwa vyama vya siasa vina Wenyeviti wakongwe wamekaa miongo na miongo, wamehasimiana huko nyuma. Hata hivyo hakuangalia historia zote, akasema ni lazima tukae pamoja, ni lazima tuanze mwanzo. Ilikuwa ndiyo Rais Samia kama ni kupoteza alikuwa anapoteza. Maana yake aliamua kwamba pamoja na yote yaliyotokea tunataka sasa nchi yetu tuheshimiane katika demokrasia.

Mheshimiwa Spika, katika jambo hili Mheshimiwa Rais amefanya vizuri sana, amewaunganisha Watanzania wote. Nataka niseme katika jambo la kusamehe ni jambo gumu. Mfano tu mdogo, Mheshimiwa Rais amesamehe mambo mengi na amekubaliana na hoja za wapinzani walizokuwa wanasema. Akiwa kwenye Mkutano wa Chama cha Demokrasia wa Wanawake lugha kubwa aliyoongea ni kwamba tusameheane, lakini wenzetu walisema kuna wenzetu 19 hatuwezi kuwasamehe, tuone namna ya kusameheana ilivyo ngumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kusema wengine walienda gerezani sijui na wengine walifanyaje, Rais akasema yote hayo tusameheane, lakini wale wakasema wenzetu 19 hatuwezi kuwasamehe asilani. Kwa hiyo tunampongeza Mheshimiwa Rais kwa moyo wa kuthubutu na kwa moyo wa kusamehe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka nije kwenye suala la uchumi. Mheshimiwa Rais alichukua nchi hii ikiwa na miradi mikubwa. Kwenye reli sote ni mashahidi na mambo mengine. Hata hivyo, tumeshuhudia namna ambavyo miradi yetu imeendelea hakuna namna ambao ulilala ha hili vile vile tunampongeza Rais wetu kwa maana ametuvusha na nchi yetu imeweza kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika diplomasia, sisi tumekaa vizuri, vita ya Ukraine na Russia ni vita ya nadharia katika diplomasia. Ni nani anataka kuwa mbabe na nani anataka wengine aweze kumfuata. Hata hivyo, sisi hapa tumepita vizuri na tumeshikilia msimamo wetu kwamba Tanzania haifungamani na upande wowote na heshima yetu inaendelea kuwepo na tumeendelea kusonga mbele.

Mheshimiwa Spika, vile vile niseme kwenye suala zima la kujenga taasisi, kilichotokea juzi kwenye ripoti ya CAG bado tuna shida ya kujenga uwezo wa kitaasisi. Yale yote ambayo Mheshimiwa Rais amesema tena kwa hasira kubwa ni kwamba wale wote wanaokabidhiwa taasisi za kuiongoza nchi hii ni lazima wawajibike vilivyo na ni lazima wafanye kazi vilivyo. Nakubaliana na Mheshimiwa Profesa Kitila Mkumbo kwamba Bunge hili lipewe nafasi lisimuonee mtu, lakini ni lazima tutajane, ni lazima tusemane na kwa mazingira ya Rais wetu alivyo, si lazima mpaka ufikishwe hatua ya kutenguliwa. Wapo watu ambao wamefanya makosa hayo, kwa hiyo kwa heshima ya Rais waweze kujiuzulu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua nafasi hii kwa dhati nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia kwenye Bajeti hii ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, ningependa nichangie maeneo matatu. Kwanza ni suala zima la kilimo katika Mkoa wa Dodoma, lakini suala zima la ukuaji wa viwanda hapa nchini na suala la utoaji wa huduma za elimu na afya hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana nilirudia katika mchango wangu kwa Wizara ya Kilimo kwamba Mkoa wa Dodoma ni lazima uchukuliwe kwa hali ya tahadhari kwa upekee ulionao kwamba hatupati mvua ya kutosha. Kwa kweli tumekuwa wahanga kila mwaka sisi hatupati mvua za kutosha na mwaka huu vile vile hatujapata mvua za kutosha na mwakani hatutapata mvua za kutosha na 2025 hatutapata mvua za kutosha kutokana na hali yetu ilivyo hapa.

Mheshimiwa Spika, nimekuwa na challenge mara nyingi kwamba tunahitaji tuwe na sera ya kilimo katika maeneo kame ikiwepo Mkoa wa Dodoma. Mkoa wetu nataka niseme Serikali bado inahitaji nguvu kuwekeza. Tunapata mvua kidogo kama nilivyosema, lakini ukija kwenye suala la pembejeo sisi tumekuwa siyo watumiaji wa mbolea kwa utamaduni wetu na ni kwa nadharia mbalimbali. Tunapata mvua kidogo, ukiweka mbolea ile itabaki pale pale juu na mimea itakauka. Kwa hiyo sisi hatutumii hii mbolea ya kemikali na tunatumia mbolea ya chumvi chumvi. Sasa kikubwa tunachofanya tunalima mazao yanayostahimili ukame; mtama mfupi umefanyiwa research unastahimili sana Dodoma unaweza ukachukua miezi miwili tayari ukawa umeiva, lakini mbegu hatupati. Mwaka jana nimefanya kampeni kubwa kwenye jimbo langu kuhamasisha wakulima walime mtama mfupi na tukawaorodhesha wakulima ili kila mmoja apate kiasi cha mbegu anachotaka kulima.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hiyo, hatukupata mbegu. Tumefuatilia kwa wakala wa mbegu na jibu tulilopata kwamba mbegu hamna. Kwa hiyo maeneo mengine wanavyokuwa na utaratibu wa mbolea za bei nafuu za ruzuku kwetu sisi hakuna. Nataka niseme Serikali ilichukue kwa dhati kuona namna gani ya kuinua suala la kilimo katika mkoa wetu. Nachelea kusema tumetelekezwa, kama tumeachwa vile, tunajilimia tu. Kwa Mkoa wa Dodoma, naomba Serikali na hata bajeti inayokuja ya kilimo ioneshe nia thabiti kabisa ya kwenda kuinua kiwango cha kilimo katika mkoa wetu. Fedha inayokuja kwenye bajeti ni fedha ya uendeshaji na uratibu, lakini katika pembejeo bado hatupati kabisa katika kuinua kilimo chetu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine Dodoma sisi tunastawisha zabibu na zabibu imekuwa ni mkombozi. Bahati mbaya zao hili limekosa usimamizi na nataka kujenga hoja hapa kwamba kuwe na Bodi ya Zao la Zabibu. Zao la zabibu liko sasa chini ya Wizara ya Kilimo, lakini Wizara ya Kilimo ina mambo mengi, zao hili limekuwa halihudumiwi vizuri. Tuunde Bodi ya Kilimo na hili Bunge wengi wamepita wanaomba Bodi ya Kilimo. Tuna Bodi nyingi za Kahawa, za Chai, kwa nini Bodi ya Zabibu imekuwa ni mtihani mkubwa? Ikishaundwa Bodi itafanya mambo yake, itafuatilia yenyewe kilimo lakini vile vile hata kufuatilia masoko.

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la mchuzi wa zabibu, Serikali imekuwa ikitoa fedha kwamba iwezeshe wanunuzi, lakini kuna curtail kwenye suala hili. Wako wanunuzi wanapewa fedha wanazunguka zunguka kununuanunua lakini hawanunui ile zabibu kwa wakulima na hata ule mchuzi kwa wakulima hawauchukui, bali ipo namna wanayoifanya. Wanachofanya wanaagiza concentrate ya unga hapa nchini lakini wanasema tumenunua. Ukiwauliza wanasema Vumi tumenunua kwa wakulima kiasi hiki, Chibelela kiasi, Mpunguzi kiasi hiki. Nenda kaulize mkulima aliowauzia, hakuna. Serikali bado inaagiza, inaruhusu concentrate iingie hapa kwetu nchini. Sasa zabibu itakua? Kwa hiyo suala hili ninachotaka kusema curtail ipo kwenye suala la zabibu na tunaomba Bodi iundwe tuwe na Bodi ya Zao la Zabibu. Nataka niwahakikishie kwamba kilimo cha zabibu kitainuka na biashara ya zabibu itasonga mbele.

Mheshimiwa Spika, suala lingine mwaka jana nilichangia kuhusu kukua kwa kutokutabirika kwa bei ya cement hapa nchini. Wote tunaweza tukachukua historia, sukari imetusumbua sana nchini, lakini kwa sasa uhakika wa bei ya sukari kutokupanda tumeshadhibiti. Kwenye cement bado hivyo hivyo kwamba cement haina uhakika na shida iliyopo ni kwamba ipo kampuni kubwa ina utaratibu wa kufunga kiwanda kwa ajili ya matengenezo na huwa inafunga mwezi wa 11 na bei ndivyo inavyopanda. Suala hili hatuwezi kuruhusu nchi yetu ikaenda namna hiyo. Kwa hiyo tuna uhakika na mwakani tena cement itapanda.

Mheshimiwa Spika, nimepitia kwenye magazeti wiki hii, ipo tatizo kwamba Kampuni ya Twiga Cement inataka kufanya acquisition ya Tanga Cement na bahati mbaya wamepelekana mahakamani, lakini na chombo chetu cha Serikali nacho kiko humo, The Fair Competition. Sasa ninachotaka kukiona katika jambo lile, nimesoma sana makala zile na nimeelewa kwamba anapokuja kuchukua share kubwa, lipo tatizo hili tunaloweza kulipata kama nilivyoelezea la mwezi wa 11. Kwa hiyo hapa tunakuwa na mzalishaji ambaye anaweza kuamua na kupanga bei yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ujenzi wa Taifa letu wananchi kupata nyumba bora, hawawezi wakajenga makazi bora kama bado cement ni bei ya anasa. Kwa hiyo jambo hili naomba liangaliwe na suala hili la sakata kati ya Tanga Cement na Twiga Cement basi tupate maelezo watu waweze kulielewa.

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa msemaji taarifa kwamba kwa mujibu wa sheria ya Fair Competition Act sikumbuki ni kipengele gani lakini kimezuia monopoly ya kampuni moja kuwa na market share ya zaidi ya 36. Merger anayoizungumza ya kiwanda hiki kinachotaka kumnunua mwenzake inakwenda kuzidi sheria tuliyoipitisha ya Bunge ya market monopoly. Kwa hiyo kwa namna yoyote lazima Watanzania watakwenda kuumizwa kwenye bei ya cement.

SPIKA: Mheshimiwa Kenneth Nollo unaipokea taarifa hiyo?

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hii na nimepewa maelezo mazuri ya kisomi zaidi, nilikuwa naongea layman kwa ujumla lakini nashukuru kwa taarifa ya Mheshimiwa Kingu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nataka niipongeze sana Serikali katika ujenzi wa majengo kwa ajili ya kutolea huduma za afya na elimu. Majengo yale tumejenga bahati mbaya kwenye elimu walimu bado hatujapeleka. Zipo shule shikizi tayari tumejenga. Ukienda kule sehemu inaitwa Mangwe Mnarani unaenda Ipole kule Igugule, unaenda Iyumba kule Nondwa majengo yapo lakini hamna Walimu. Hivyo hivyo zahanati nyingi zimejengwa katika vijiji kwenye jimbo langu lakini hakuna wahudumu wa afya. Kwa hiyo, naomba Serikali wananchi wana shauku kubwa ya kupata afya na kama ni majengo wameyaangalia kwa miaka miwili, wameshangaa vya kutosha sasa wanahitaji kupata huduma ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa nataka niipongeze kwa dhati Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Kilimo. Wamefanya kazi nzuri katika kutuletea mahindi ya bei nafuu. Kwa Wilaya ya Bahi nimekuwa mnufaika mkubwa sana. Kila kata imeweza kupata mahindi yale ya bei nafuu na nataka niseme utaratibu huu kwa kweli sisi ambao nimesema hali ya kilimo bado haijaimarika na mwakani uweze kuendelea, kama nilivyosema mwaka huu hatujapata mvua za kutosha, kwa hiyo Serikali iendelee na utaratibu wa kuweza kutupatia mahindi ya bei nafuu, lakini kikubwa zaidi iweze kuangalia namna gani inaweza kusaidia mkoa wetu katika kuinua kilimo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nianze kwa kunukuu kupitia Karl Marx na Engels wote wanakubaliana kwamba, naomba kunukuu kwamba “Despite the capitalist economy, the economic modes of production define the class structure of the society.” Pamoja na kwamba na mfumo wa kibepari lakini mfumo uliopo wa kiuchumi katika jamii fulani unatoa madaraja ya jamii ile kwamba namna gani ilivyokaa katika uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiangalia katika nchi yetu tukiweza kuwapanga wafugaji kwenye mfumo wetu wa uzalishaji na mfumo wetu wa uchumi, wafugaji ndiyo wanaotokana katika daraja la mwisho zaidi la uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua kigezo kwamba mfugaji hakopesheki kwenye mabenki na tukianza na wafanyabiashara wakubwa wenye viwanda wanakopesheka kwenye mabenki. Wafanyabiashara wa kawaida wachuuzi wanakopesheka kwenye mabenki lakini siku hizi tumeweka na wajasiriamali na wamachinga humo humo wanakopesheka kwa kiasi fulani kwenye mabenki. Wanakuja wakulima wanakopesheka kwenye mabenki lakini mtu ambaye hakopesheki kwa sababu ya kutokuwa na anwani ni mfugaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo kwamba tu lakini ni namna gani sisi wenyewe tumemtengenezea mfugaji asiaminike, mfugaji asikopesheke na mfugaji asiwe na anwani. Nataka kusema kwamba nchi yetu tuna mifugo mingi na tuna wafugaji wengi lakini kwenye uzalishaji bado hatambulilki katika mfumo wa kiuzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Serikali ilikuja na utaratibu wa utambuzi wa mifugo ile inaitwa Ear tag Electronic System. Mfumo huu umefanikiwa sana katika Nchi ya Botswana kwamba mifugo inavyozaliwa baada ya miezi mitatu anapewa electronic tag na ile electronic tag inakuwa na habari mbalimbali. Aina ya mifugo, inamilikiwa na nani lakini vilevile kwa ajili ya kupata dawa, traceability na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kinachosababisha wafugaji wetu wasiweze kukopesheka ataenda benki anataka kukopa lakini benki wanataka wajue ana mifugo kiasi gani? Sasa mifugo kiasi gani ni lazima kuwe na mfumo ambao unatambua kwamba ana mifugo kiasi gani ambayo imethibitishwa na mfumo halali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mfugaji huyu akienda kutaka kukopa baada ya siku mbili, tatu anahama kutoka Shinyanga anaenda Mtwara kwa hiyo hata benki haiwezi kumkopesha. Kwa hiyo, nilichotaka kusema ni kwamba Serikali mfumo huu ni lazima kama ilivyousitisha iurejeshe. Jambo la msingi Serikali iongeze ruzuku kwenye zoezi ili kwamba wafugaji wetu waweze kusajili mifugo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni zuri kwamba Serikali itakuwa inapata mapato kwa sababu mfugaji anavyoenda kuuza inawezekana kukawa kuna namna gani anaweza kuchangia katika kulipia ushuru mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi, jambo hili limezungumzwa kwamba katika mwaka 2025 kutakuwa na utambuzi wa mifugo. Kwa hiyo, jambo hili lipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nataka kwa dhati niipongeze Wizara ya Mifugo. Wizara hii imekuwa haipati fedha za kutosha. Bajeti ya mwaka huu ina bilioni 290 tu, ambayo ni kidogo sana. Ukienda Taasisi ya Utafiti wa Mifugo TALIRI ina fedha haizidi bilioni moja; yaani taasisi ya kufanya utafiti wa mifugo haipati fedha, hata bilioni moja haifiki. Kwa hiyo naomba Serikali iangalie sana, kwamba sekta hii ya mifugo iweze kutoa fedha. Na nataka niipongeze Wizara hii, imefanya kazi kubwa ambazo pamoja na kupata hela kidogo lakini wameonesha uwezo mkubwa wa kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, kinachowaangusha wafugaji wetu ni kwamba maeneo ya malisho hayajapimwa, na tukiri kwamba Wizara ya Ardhi ina sura ya Wizara ya migogoro ya ardhi, si Wizara ya kupima maeneo. Sasa kama inawezekana itengenezwe mamlaka kwa ajili ya upimaji wa maeneo ya mifugo, mamlaka ambayo itashirikisha kati ya Wizara ya Mifugo na Wizara ya Ardhi ili kwamba wafugaji wetu waweze kupimiwa maeneo na waweze kuweza kulisha mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikwambie jambo hili limeshuka hata maeneo yetu tunayokaa; wafugaji wanaishi kwa kutangatanga. Njia ya wafugaji kiasili zilikuwepo tangu zamani, siku hizi watu wanaamua kulima hata njia za wafugaji, tunaita mapalio, hamna mapalio sasa, kwa hiyo mfugaji anaishi kwa kutangatanga, naomba jambo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusu suala la majosho na maji, mabwawa, malambo, jambo hili nalo liangaliwe. Mimi Kata yangu ya Chifutuka ina ng’ombe zaidi ya 2,500 lakini hakuna sehemu ambapo mifugo inaenda kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongea sekta hii lakini hii ni sekta ambayo kwa kiasi kikubwa tumeitelekeza. Bado tunachukulia kwamba mfugaji ni mtu ambaye yuko kienyeji na Serikali bado haijaangalia suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nataka nimpongeze kwa dhati Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, kwanza kwa kuanza kiufufua Ranch ya Kongwa na mwaka jana kulikuwa na tatizo la kutaka kuibadilisha ranchi yawe mashamba ya alizeti. Kwa vitendo amefanya, amepeleka matrekta matano, amepeleka ng’ombe 1000 kwa hiyo huko ndiko tunakoelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Waziri na nataka niseme nchi yetu ina utajiri mkubwa wa mifugo, masoko yameshafunguka sasa, kama vile Saudi Arabia, Vietnam na kwingineko, tutumie fursa hii. Ng’ombe wa Tanzania walikuwa hawauziki kwa sababu hatuna traceability, kwamba huyu ng’ombe ametibiwa haijulikani, na ndiyo maana wenzetu wanaangalia namna gani nyama yetu inavyokuwa. Kwa hiyo tayari tuko katika nafasi nzuri kuendelee kuipatia fedha Wizara hii ili iweze kujiendeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu migororo ya wafugaji na hifadhi zetu. Mimi wiki iliyopita ng’ombe 191 walikamatwa wameingia kwenye hifadhi, na bahati mbaya walivyokamatwa inatakiwa ng’ombe mmoja alipiwe laki moja. Sasa utaona kiasi gani mkulima huyu mfugaji anaweza kutoa. Lakini chanzo cha kwenda kwenye hifadhi ni nini? chanzo cha kwenda kwenye hifadhi ni kutafuta malisho. Kwa hiyo Serikali iangalie, kama nilivyosema mwanzo, namna gani inaweza kudhibiti tatizo hili la wafugaji kupeleka ng’ombe kwenye hifadhi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kuunga mkono hoja hii ya Wizara ya Kilimo, lakini vile vile nataka kwa dhati kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa nia njema aliyonayo katika kukuza kilimo cha nchi yetu. Kama tunavyofahamu mwaka juzi uliopita bajeti ya kilimo ilikuwa karibu bilioni 300, lakini mwaka huu ambao unaisha bajaeti ya kilimo ikaongezeka kuwa bilioni 751, lakini mwaka huu bajeti ya kilimo imekuwa bilioni 970. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sio hilo tu ukiangalia utekelezaji wa bajeti hii unaona kabisa kwamba fedha inatoka na utekelezaji hadi sasa ni asilimia 73.2 na huko nyuma ilikuwa ni asilimia 51, 49, 50, ni hapo hapo, lakini safari hii inaenda hadi asilimia 73. Kwa hiyo kwa kiasi kikubwa nataka niseme Wizara hii kazi kubwa inafanyika nampongeza sana Mheshimiwa Waziri amekaa kimkakati lakini vile vile nimpongeze sana na Naibu Waziri Mheshimiwa Mavunde lakini vilevile nataka nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Mkurugenzi wa Umwagiliaji. Tunaona kabisa lengo kubwa la kutaka kuendeleza kilimo cha umwagiliaji na kuinua kilimo katika nchi yetul inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la umwagiliaji katika nchi yetu ni takribani milioni moja na laki mbili. Hadi sasa tunamwagilia kiasi cha hekta 727,000. Kwa hiyo bado tuna kazi kubwa na bado Wizara hii ipewe fedha za kutosha ili tuweze kufikisha lengo la Watanzania la kuwa na chakula cha uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichukue nafasi hii vilevile kuishukuru sana Serikali, Wilaya yangu ya Bahi ilikuwa imeathirika sana na upungufu wa chakula, lakini kupitia NFRA tumeweza kupata chakula karibu kata zote na jumla ya tani 1,530 zimegaiwa katika kata zote. Jambo hili kwa dhati naishukuru Serikali. Kupitia hapo nataka nimkumbushe Mheshimiwa Waziri nimeangalia katika mpango ule wa kugawa mbegu, ipo alizeti lakini mtama mfupi haupo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana Mheshimiwa Waziri kwa dhati kabisa atuangalie hasa kanda ya kati na jambo hili nimekuwa nalisema sana kwamba, bado tunahitaji mtama mfupi ambao ndio mkombozi katika eneo letu. Hatupati mvua za kutosha. Kwa hiyo, pamoja na kwamba Mheshimiwa Waziri ametupatia alizeti naomba sana Mkoa wa Dodoma uwe na special treatment tuweze kupata mbegu ya mtama mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuja kwenye suala zima la BBT; jambo hili ni zuri, lakini yapo mambo ambayo naona lazima tuyarekebishe. Kwanza eneo hili tumewapa vijana ambao hawana ajira, tunataka kuwakomboa, lakini tunataka walime mazao ya muda mrefu. Zabibu inachukua miaka mitatu ili aweze kuvuna, hali kadhalika na korosho nayo nasikia inaenda miaka mitano. Sasa Mheshimiwa Waziri hapa tunafanya kama ni rescue plan. Sasa kijana huyu ambaye atasuburia miaka mitatu wakati hana ajira, mkakati huu nauona kama hauendi sawa sawa. Vile vile kwenye umilikishaji tulisema kwamba vijana hawa watamiliki kwa miaka 66. Sasa kijana ambaye ana miaka 30 leo unataka amiliki kile kieneo kwa miaka 66 atakuwa babu tayari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ni lengo la kuhamasisha na kutoa ajira kwa vijana, nashauri iwe miaka 10 hadi 15. Ili kwamba ikishapita miaka 15 amesha-graduate ili tuchukue vijana wengine na ikiwezekana Mheshimiwa Waziri yasiwe mazao ya muda mrefu, yawe mazao ya muda mfupi. Kwa sababu kwanza ukiangalia katika nchi yetu hatujapata uwekezaji kwenye nafaka, sasa tukiweka katika suala hilo ina maana tutaweza kupata watu wa nafaka lakini vile vile vijana wetu wakapata fedha kwa muda mfupi na iwe ni program ya miaka 15 ili akisha-graduate na wengine waweze kuendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nije kwenye suala la zabibu; mkoa wetu ndio pekee ambao unastawisha zabibu kwa kiasi kikubwa. Nimesema suala la Bodi ya Zabibu, naomba sana na namhakikishia Mheshimiwa Waziri nitashika shilingi, nataka aje na majibu ya kuanzisha Bodi ya Zabibu. Nasema hilo kwa nia njema tu, Wizara ya Kilimo ina mambo mengi, zao la zabibu kuwa chini ya Wizara ya Kilimo, kidogo kuna kuwa na mambo mengi. Sasa tunakosa umadhubuti wa kuweza kulikuza zao hili. Kama mwaka huu ukiangalia uuzaji wa zao la zabibu bado haueleweki. Viwanda vingi vinasema havitanunua na havitanunua kwa sababu kwanza bado wana mchuzi ule kwenye maghala yao, lakini vile vile bado uhakika wa soko hauko kwa wakulima. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri naomba majibu ya kutosha akija kwenye suala hili la zabibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, amenipa Mradi wa Umwagiliaji pale Kongogo wa bilioni tano na milioni 600. Haijawahi kutokea katika Wilaya ya Bahi kupata fedha hizi kwa pamoja, nakushukuru sana na naipongeza sana Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine naomba, tuna skimu yetu kubwa sana ya umwagiliaji ya Bahi na tumeunganika na Kintinku. Mwaka jana Wizara ilisema wanafanya upembuzi yakinifu na mwaka huu tena naona upembuzi yakinifu. Namwomba Mheshimiwa Waziri, watu wa Bahi wanasubiri ukarabati wa skimu ile na kama anavyofahamu, kama nilivyosema Bahi na Kintinku, tunategemea zaidi mabonde haya kwa maisha ya watu wetu. Mji wa Bahi unategemea zaidi suala zima la kilimo cha mpunga. Kwa hiyo naomba badala ya upembuzi yakinifu, twende kwa haraka ili kwamba ikiwezekana mwaka huu unaokuja tuanze ukarabati ambavyo mwanzo nilikuwa najua itaweza kufanyika hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri ametaja kukarabati Skimu ya Chikopelo, Skimu ya Mtitaa, Skimu ya Mkakatika, lakini jambo kubwa zaidi nataka niseme kwenye suala zima la skimu zetu. Maeneo mengi ambayo maji tunatenga kwa mfano Skimu ya Kongogo ile tutalima mwaka mzima. Kwa hiyo na skimu nyingine hizi tukiweka utaratibu kwamba tuwe na uhakika wa kulima mwaka mzima tutakuwa tumewaokoa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, napenda tena nichukue nafasi hii kuiunga mkono hoja na nampongeza Mheshimiwa Waziri. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuweza kuchangia bajeti ya Wizara hii muhimu, lakini pia nataka nikuahidi kwamba nitaenda hoja kwa hoja.

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa umeme nchini ipo katika sura mbili. Sura ya kwanza ni utekelezaji wa miradi mikubwa ya kuzalisha umeme lakini vilevile na miradi mikubwa ya kusambaza umeme. Sura ya pili ni kuunganisha umeme kwa watumiaji; ndivyo ilivyo hali ya upatikanaji umeme.

Mheshimiwa Spika, mimi nataka nijikite kule kwenye kuunganisha umeme. Hali ya kuunganisha umeme kwa watumiaji bado si nzuri; na siasa kubwa ya umeme kule kuwaunganishia watumiaji hali yetu bado si nzuri.

Mheshimiwa Spika, mimi kwenye jimbo langu vijiji vyote vimepata umeme lakini vitongoji takriban vyote havina umeme. Na bahati mbaya REA walikuwa wakishafikisha kwenye Kijiji wanalambisha umeme basi, kisha wanaondoka. Na kitu ambacho nashangaa hata zile scope nani alikuwa anaenda kukagua? Maana yake ni mtaa mdigo unalambishwa na kijiji kiwe tayari kina umeme.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mawili ambayo mimi nataka Serikali iwe bold. Suala la gharama ya kuunganisha umeme kwa 27,000 hebu Serikali ilijadili jambo hili, je, ni jambo la kiuhalisia? Maana sisi tumesema sana kwenye mikutano kwmaba umeme ni 27,000, lakini uhalisia siyo 27,000. Serikali iseme, kama inatakiwa kiasi fulani iseme kwa uhalisia wake. Wananchi wanajiunganishia umeme wanaweka ile connectivity ndani, kwa maana ya miundombinu, lakini akija kwenye kuunganishiwa 27,000 wanaambiwa kuna nguzo moja inatakiwa ije kwako inabidi utoe 300,000. Jambo hili wananchi wanashindwa kuelewa. Lakini mentality ya TANESCO inaangalia, kwamba kitongoji kile kina watu wachache na hivyo tukipeleka umeme hatina wateja. kwa hiyo kuna conflict hiyo.

Mheshimiwa Spika, mimi nashauri kuwe na muundo mathubuti, muundo wa kwanza REA iendelee na shughuli ya miradi mikubwa, iwe kama na sura ya TANROADS, lakini vilevile tuwe na Wakala wa Umeme Vijijini ambaye sasa ata-deal yeye na ku-connect kwenye vitongoji atafute nguzo atafute transformer ili kazi ya kuunganisha aifanye yeye; lakini anayehusika na wateja ni TANESCO.

Mheshimiwa Spika, TANESCO sasa yeye ni kuangalia namna gani anaweza kupata fedha baada ya wananchi kuunganishiwa umeme. Tukienda na muundo huu hali yetu ya upatikanaji umeme na kuunganisha umeme kwa wananchi itakuwa imekaa sawasawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuwe na REA ambasyo itakuwa na sura kama ya TANROADS lakini tuwe na Wakala Umeme Vijijini ambaye atakuwa na sura kama ya TARURA halafu TANESCO yeye a-deal sasa na masoko, namna gani anaendesha Wananchi wapate huduma ile sasa ya umeme.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba Serikali ikiwezekana wakati Waziri ana wind up tupate uhakika kwamba 27,000 inakidhi au 27,000 haikidhi? Kama kuna kiwango ambacho tunaona inafaa basi ipendekezwe na wananchi wataona kweli hiki kina uhalisia, lakini tunavyoenda hivi kila mmoja anamdanganya mwenzake, sasa hatuwezi kwenda na utaratibu huo.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ni kuhusu suala la nishati ya umeme katika maeneo mbalimbali (power mix). Private sekta inakuja na miradi kama ya solar kutaka iweze kuiuzia TANESCO umeme. Lakini mimi nataka niseme pamoja na sera yetu kusema hivyo lakini kuna uzito mkubwa sana. Ili kuja kupata mradi wa solar uiuzie TANESCO it takes ages, na ni ngumu kweli kweli. Sasa turuhusu watu waje tupate umeme wa kutosha watu waweze kujiunganishia. Lakini ni jambo gumu kweli kweli kwa mtu mwenye kutaka kuzalisha ueme lakini hata tariffs ambazo inatakiwa walipe haziendani na namna ambavyo wameweza kufanya kazi ya kuwekeza hili suala hilo; kwa hiyo nilikuwa naliomba hilo.

Mheshimiwa Spika, jambo jingine ni kuhusu upatikanaji wa vifaa. Kinachosumbua tusiunganishiwe umeme vijijini ni kukosekana kwa transformer na kukosekana kwa nguzo. Haijulikani, na ndilo jambo gumu. Kule kwenye ofisi za TANESCO wanasubiri wapate nguzo, wanasubiri wapate Transformer, transformer hazipatikani. Sasa jambo hili kuna kipindi tulizuia hakuna transformer kutoka nje zitengenezwe hapa ndani. Sasa Mheshimiwa Waziri aje atuambie kama tunaruhusu transformer zije kwa wingi lakini na shida ni nini, nguzo tunazalisha hapa kwetu, na zenyewe nazo tulizuia kwamba zisitoke nje ya nchi kama inawezekana nguzo zije za kutosha za ndani ya nchi na hizo zitakazotoka nje ili kwamba kuwe na uhakika wa kupata nguzo, hapo ndiyo tutaenda kila kitongoji kitapata umeme.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo lengo la Mheshimiwa Waziri, hata mwaka jana, alitaka vitongoji vyote vipate umeme. Lakini kuna uzito, hata hivi 15 bado ni vitone vya maji. Kwa hiyo, jambo hili nalo tuliangalie ni namna gani tunakuja na utaratibu madhubuti, kwanza kimuundo, kwa maana ya kuwa na wakala wa usambazaji wa umeme vijijini lakini REA yeye awe na sura nyingine ya TANROADS.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo jingine ni kuhusu usambazaji wa gesi. Mkoa ambao unakula mkaa kwa wingi ni Mkoa wa Dar es Salaam. TPDC wana mradi wa kusambaza umeme kwenye nyumba, lakini jambo hili nalo haliendi sawa sawa. Serikali iangalie, kama TPDC hawezi basi apatikane muwekezaji ambaye ataweza kufanya kazi ya kusambaza umeme. Kufanya hivyo tutazuia matumizi ya mkaa kwenda Dar es Salaam na tutailinda miti yetu. Kwa hiyo jambo hili nalo liweze kuangaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine, nimepitia maoni ya Kamati. Kamati inaongelea habari ya kwamba TBS kwenye suala la vinasaba ipewe uwezo, ijengewe uwezo wa kutosha na ipewe muda ili iweze kuja na utaratibu wake. Jambo hili ni zuri; lakini kwa maana nyingine tena tayari tender imetangazwa kwamba ipatikane kampuni ambayo inaweza kufanya kazi ya vinasaba. Kwa hiyo kuna contradiction kati ya Kamati lakini mimi nachotaka kusema hali ambayo TBS ilichukua, ilichukua katika wakati mgumu sana na jambo hili TBS wamejitahidi. Sasa kama Serikali inaona ipo haja tuone kwa nini tunatoka tunamuacha TBS ambaye katupitisha kwenye kipindi cha mpito kama kuna mambo ya kurekebisha basi yaweze kurekebishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zaidi mimi naipongeza sana Serikali kwa uwekezaji mkubwa wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Sisi sasa katika ukanda huu wa Afrika hasa hasa Kusini mwa Afrika tunaingia katika idadi ya nchi ambazo zina umeme mkubwa na tunaweza kusambaza nje. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri. Wizara hii ni kubwa, ina mambo mengi na Wizara yenye mapambano mengi; lakini anafanya kazi kubwa na aendelee kufanya kazi kubwa ili kwamba Taifa letu liwe na umeme wa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu asilimia 23 ya ardhi ndiyo inayotumika katika kilimo. Nchi yetu ina watu milioni 40 ambao wanajihusisha katika kilimo. Kwa hiyo, ukiangalia Sekta ya kilimo ndiyo sekta kubwa inayoajiri, ndiyo inayotegemewa katika maisha yetu katika ustawi wa Taifa letu. Kwa hiyo, nilitaka kusema jitihada za Mheshimiwa Waziri ni nzuri, lakini ukizipima siyo jitihada za kimapinduzi, bado dira ya kimapinduzi ya kuboresha kilimo chetu na kwenda katika malengo hasa ya kuliendeleza Taifa hili bado, nimeangalia hii bajeti kuna eneo bado hatujakaa sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri amerejea Awamu ya Kwanza Awamu ya Pili na Awamu ya Tatu. Nilitaka rejea ileile ya kuanzia Awamu ya Kwanza na kuishia Awamu ya Tatu. Awamu ya Kwanza tuliamua kwamba kilimo cha nchi yetu kiwe ni kilimo cha wakulima wadogo wadogo, lakini tuliamua kwamba wananchi watengenezewe viwanda ambavyo vitahudumia kilimo chetu. Kwa bahati mbaya Awamu ya Tatu tukaja tukabinafsisha viwanda vya kuhudumia kilimo, vilevile tukabinafsisha mashamba makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilitaka kusema na ili nimshauri Mheshimiwa Waziri Bashe, kwamba pamoja na jitihada zake kubwa ni lazima tuamue tunafanya kilimo cha wananchi wengi au tunataka kufanya kilimo cha kibepari au tunataka kuunganisha kilimo cha wananchi wengi pamoja na ubepari. Ninasema hivyo kwa sababu gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija katika hoja ya msingi ukitaka tulete makampuni makubwa, kampuni kubwa inahitaji uwe na eneo kubwa, Wilaya nzima ya Bahi unaipa kampuni kubwa iweze kulima na iweze kusafirisha. Lakini kwa wananchi wetu katika umoja wao, unaweza ukawaunganisha ukawatengenezea ushirika mzuri na tukaweza kulima kwa pamoja na tukawa na viwanda vya kutuhudumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa ambalo naliona katika nchi yetu bado tunapandishia mifumo, tunachukua mfumo wa Kimarekani tunachanganya na mfumo wa China na mfumo wa Vietnam hatuwezi kusogea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu kwa mfano Vietnam, Vietnam sasa ndiyo inayouza mchele ukijumlisha mchele wa Afrika wote katika ku-export hauwezi kuifikia Vietnam nchi ndogo. Wenzetu wamefanya katika maana ya ushirika, vyama vyao vya Ushirika vina nguvu. Kwa hiyo, kazi ya Serikali kwanza itoe fedha katika ku-finance agriculture ambapo tumeanza kwenye umwagiliaji kwa kiasi kikubwa lakini vilevile ushirika wetu tuimarishe, mahusiano ya Serikali na Ushirika usiwe kama Polisi na mtuhumiwa! Kwenye Ushirika bado kuna shida hakuna Uongozi. Kwa hiyo, nilitaka kwanza hiyo contradiction Wizara ya Kilimo na Serikali waweze kuiangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nilitaka nichangie kuhusu Kanda ya Kati. Kanda ya Kati tuchukulie kuanzia Mkoa wa Tabora, Wilaya za Nzega kuja Singida na Dodoma, bado Serikali haijawekeza kwenye kilimo! Hali ya chakula bado ni mbaya, tunasumbuliwa na ukame, lakini bado hatujawa na sera madhubuti kwamba ni namna gani tunasaidia kilimo katika Kanda ya Kati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu Nigeria walianzisha sera ya maeneo yenye ukame na wamefanikiwa kwa kiasi kikubwa. Kwa hiyo sisi bado, pamoja na hisi skimu ambazo mmetuletea nazo nilikuwa nazihesabu ni kidogo mno lakini bado suala la Kanda ya Kati hatuja-address kilimo hiki, bado kuna dilemma kubwa kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa niseme kuhusu suala zima la zabibu. Mimi nimekua katika miaka ya 1980 tulikuwa tunalima sana zabibu, bahati mbaya zabibu ikaja ikafa kwa maana ya kuharibu kile kiwanda na tukakosa soko Zaidi, lakini sasa….

MWENYEKITI: Malizia sentensi ya mwisho.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iamue kuwekeza kwenye zabibu, kiwanda chetu cha DOWICO kirudishwe lakini tuanzishe bodi ya kusimamia zao la zabibu, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi; awali ya yote kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri wa Mifugo na Naibu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wizara hii sote tunaijua kwa nyakati nyingi imekuwa ni wizara ambayo haipewi kipaumbele, lakini wizara muhimu sana katika nchi yetu kwa maana inachangia pakubwa katika pato la Taifa. Nimeona jitihada nyingi sana za Mheshimiwa Waziri ambazo anazifanya katika sekta ya mifugo ikiwa kwenye ujenzi wa majosho. Wilaya yangu ya Bahi tumeweza kupata majosho nane katika mwaka wa fedha 2021/2022 na huko nyuma ilikuwa ni nadra sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kuja na mfumo wa kuwa na hereni za kieletroniki jambo hili limefanyika sana katika nchi ya Botswana kwamba mifugo inavyopata electronic tag tayari tunakuwa tunajua taarifa ya mfugo ule lakini unaungamanisha na maeneo mengine kwa mfano TRA wanaweza kuwa wanajua taarifa za mifugo ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasaidia sana kwa maana ya kwamba mfugaji wetu sasa anaweza kwenda kukopesheka. Maana yake ana mifugo inayotambulika na utaratibu wake akiuza inajulikana kwamba ng’ombe mwenye Serial Number hii sasa ameuzwa. Kwa hiyo, haya ni mapinduzi makubwa na Mheshimiwa Waziri kwa dhati kabisa nakupongeza kwa initiative hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kuchangia katika maeneo matatu; la kwanza nianze katika suala zima la uuzaji wa nyama nje ya nchi. Nimefanya biashara hii kwa kiasi kukibwa lakini hatujawekeza vizuri katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tumezuiliwa kuuza nyama yetu katika baadhi ya nchi, tumezuiliwa kwa sababu ya uchakavu wa machinjio ya Serikali, kwa sababu ya kuwa na hali mbaya ya mazingira. Hatuwezi kuuza Saudi Arabia, hatuwezi kuuza Falme za Kiarabu na maeneo mengine, lakini unavyokosa soko la Saudi Arabia ina maana umekosa fursa yote ya Middle East. Unavyokosa soko la Falme za Kiarabu ina maana umekosa kuuza Middle East yote, tatizo liko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda chetu cha machinjio cha Kizota walikuja wataalam kukagua wakakuta kina hali mbaya, lakini kwa muda mrefu na wataalamu walishafanya tathmini hata tathmini ya hivi karibuni inatakiwa Bilioni Mbili na Milioni Mia Tano tu. Sasa Shilingi Bilioni Mbili na Milioni Mia Tano imetugharimu kwa kiasi kikubwa. Nikitaka mimi kuuza mbuzi au kondoo nje ya nchi au ng’ombe natumia viwanda vya watu wengine hapa, lakini itaonekana lebo ya mwenye kiwanda kile na siyo kampuni yangu, sasa huu ni unyanyasaji. Naweza nikafanyiwa fitina muda wowote nikanyang’anywa soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba sana Serikali na Mheshimiwa Waziri jambo hili uliahidi bajeti iliyopita, sasa Bilioni Mbili na Milioni Mia Tano kweli Serikali? tumekaa miaka Sita? Eneo lile la Kizota halikarabatiwi? Kama Serikali imeshindwa nipeni basi hata mimi! Shilingi Bilioni 2.5 ni kitu ambacho kinawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba sana Serikali kwenye jambo hili Bilioni Mbili na Milioni Mia Tano ni kitu cha aibu kukaa muda wote huo Mheshimiwa Waziri. Kwa hiyo, tunalazimika kwenda kuchinjia ng’ombe wetu Kenya, mbuzi tunachinjia Kenya, kondoo Kenya. Export ya Kenya inaonekena sasa ndiyo kubwa kwenye mifugo, lakini ng’ombe wanavuka Namanga wanaenda kuchinjiwa kule na tunafanyiwa udalali mkubwa haijawahi kutokea na masharti makubwa. Sasa Mheshimiwa Waziri kweli Bilioni Mbili zinatufanya tuwe hivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nisiseme sana na mengine yanayotokea kwenye viwanda vyetu vya hapa ndani, lakini Mheshimiwa Waziri kwenye hili kwa kweli, tusaidie kukarabati kiwanda chetu cha Kizota.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunauza ng’ombe au nyama ya mbuzi na kondoo ikiwa ni katika hali ya kawaida ya caucus, lakini hatu-process. Tanganyika Packers tulikuwa nayo, nyama yetu hatupeleki iliyo-processed, tunapeleka kama tunavyopeleka mahindi ya kwenda tu kusaga nje. Sasa Mheshimiwa napata shida na mimi niliseme sana hili la ku-process nyama kama tu kiwanda hiki cha machinjio tu ya Bilioni 2.5 tunashindwa sasa nikianza kusema na habari kiwanda cha ku-process nitakuwa naongea kitu kikubwa. Hebu na hili nalo liangalieni sasa kwamba, tuweze kuuza mazao ya mifugo nje ya nchi badala ya kupeleka ng’ombe, nyama, ambazo wenzetu wanaenda ku-process upya kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu malisho. Wafugaji wetu ni wakimbizi ndani ya nchi yao, na tunalaumu kwamba, kwa nini wanahamahama, wanahamahama kutafuta malisho, lakini umiliki wa ardhi kwa ajili ya malisho bado haujakaa sawa. Mheshimiwa Waziri jambo hili liangalieni. Nchi ya Zimbabwe imepiga hatua kubwa sana na walipata mkopo kutoka AU kwa ajili ya kuzalisha malisho, ukienda nchi nyingi za Ulaya wenzetu wameshafika hatua hiyo ya kulima malisho, habari ya kuacha ng’ombe azurure ajitafutie chakula ni kitu cha kizamani sana. Kwa hiyo, tuanze wafugaji wetu kuwatafutia maeneo kwa ajili ya malisho, pia wamiliki ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ng’ombe wetu na wanyama wetu katika soko la dunia nyama yake ni ngumu sana. Sote tunajua ng’ombe atoke Shinyanga mpaka Katavi kwa kuhamahama kwa hiyo, tunaharibu hali ya mifugo yetu, lakini kosa kubwa ni kwamba hatufanyi uwekezaji kwenye malisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni miundombinu. Ng’ombe na mifugo mingine hawapati maji, hatuna majosho. Sasa wekeni utaratibu na kama Serikali haiwezi kwenye hili, basi tuweke utaratibu wa wafugaji wetu wawe sehemu moja waji-organize waweze kufanya utaratibu wa kujenga miundombinu. Kwa hiyo, bado tuko katika karne ya kizamani. Kuna watu wengine wanasifia kwamba ng’ombe wetu hatuwatibu sana na madawa kwa hiyo ni ng’ombe wazuri. Dunia ya wapi nani anataka kula ng’ombe wana magonjwa? Anataka kula nyama ina magonjwa? Wanasema kwamba, kuku wetu wa kienyeji ni watamu, hiyo ni wrong perception. Nani anakula kuku anaumwa, anapona mwenyewe, anajitibu mwenyewe, hiyo ni nyama gani mtu anataka kula? Kwa hiyo, kwa sisi Kanda ya Kati msitupeleke kwenye hiyo habari kwamba, kuku wa kienyeji ni wazuri, tunakula wenyewe tu, lakini nani anaenda kula kuku hajawahi kutibiwa hata siku moja halafu unakula? Hivyo, nataka niseme jambo hili, hebu tutoke na mawazo ya kiufugaji wa kizamani. Dunia inabadilika, dunia inakimbia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala zima la vyuo vyetu vya mafunzo kwa ajili ya mifugo. Vyuo vina hali mbaya havipati bajeti zake, bado vinafundisha teknolojia ya kizamani, bado wana nadharia kubwa. Ukienda maeneo yale unashangaa tangu alivyojenga Mwalimu Nyerere majengo yale hayajaongezeka. Sasa kama hatuna Training Institute, hatuna researching centers nzuri za mifugo, tutabaki kusema Tanzania ni nchi ya pili katika Afrika kwa kuwa na mifugo wengi, basi ni nyimbo, lakini ukija kwenye uhalisia hali yetu ni mbaya sana, hatujawekeza kwenye mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya Wizara hii imekuwa inapata fedha kidogo sana. Nami kwa kweli, siwezi kumlaumu hata Waziri, mwaka jana ilikuwa Shilingi Bilioni 243.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nikushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia katika Wizara hii ya Mambo ya Nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa dhati nianze kuipongeza Serikali kwa namna ilivyoahidi mwaka jana kwenye bajeti iliyopita kuhusu kufungua ubalozi mdogo pale Lubumbashi, ila vilevile niipongeze kwa kufungua sasa ubalozi Indonesia. Indonesia sasa ni nchi ambayo inaelekea kuwa nchi ya nne katika kuwa na uchumi wa kilimo. Kwa hiyo, ni jambo zuri na naipongeza Serikali kwa dhati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niongelee habari ya sera ya mambo ya nje na wataalam katika masuala ya diplomasia wanasema sera ya mambo ya nje ni kitu kinachoishi yaani sera ya mambo ya nje ni kitu kinachoishi, kwa hiyo, sera zetu katika miaka ya 1980 miaka ile tunafanya ukombozi wa Afrika wakati wenzetu bado hawajapata uhuru haziwezi kulingana na leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mabadiliko yametokea katika nyanja hizo na sera ya mambo ya nje inabadilika kila wakati, inabadilika kutokana na mazingira ya dunia, lakini vilevile inabadilika kutokana na namna ya uongozi unavyokuwa madarakani. Lakini Tanzania nataka niseme tumekuwa vinara wazuri katika sera ya mambo ya nje na kikubwa zaidi ambacho tumeshikilia ni kuhusu suala la kutokufungamana na upande wowote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nitoe maoni yangu binafsi kwamba kumekuwa na maneno wakati mwingine yanatoka ndani ya Serikali kwamba miaka sita iliyopita nchi yetu kama ilikuwa imejifunga yaani kwamba sasa nchi yetu ilikuwa imefungwa, yaani haina uhusiano na nchi zingine na bahati mbaya niliwahi kunukuu hata balozi mmoja anasema sasa Tanzania inafungua milango yake baada ya kuwa na siasa ambayo ilikuwa imejifunga na international community.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kama nchi tuwe na msimamo, ni balozi gani tulifunga kwamba tumefunga ubalozi kutokana na ugomvi huo? Ni balozi gani tulimfukuza kwamba sasa kutokana na hili tumekufukuza, tumekuondoa. Kwa hiyo, tumekuwa tunajibebesha maneno kana kwamba nchi yetu iliingia kwenye mgogoro mkubwa wa kimataifa na tukafunga kila kitu, kitu ambacho si kweli. Biashara zimeendelee kama kawaida, si kwamba sasa ndiyo tumeanza biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme maneno haya, inawezekana tukawa tunabomoa kwa upande mmoja, aidha kwa kutokujua au katika propaganda ambazo zinatoka katika upande mwingine wa dunia. Kwa hiyo, nchi yetu imeendelea na sera madhubuti za kuimarisha hasa hasa uchumi na tulipofika hapa leo ni muendelezo wa kipindi chote, hakuna sehemu ambapo kama ni behewa lilikatika, tunaendelea hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme wenzangu wamechangia kuhusu diplomasia ya uchumi na kama nilivyosema foreign policy, siasa ya mambo ya nje ni siasa inayoishi. Kazi tuliyonayo sasa ni nchi yetu kuamua namna gani inaweza kukuza biashara kati ya mataifa mengine duniani. Mimi nataka niseme kuhusu Pakistan. Pakistan ni Taifa ambalo tumekuwa tunafanya nalo biashara kwa muda mrefu, mwaka 2019/2020 biashara yetu kati ya Pakistan ilikuwa kati ya dola bilioni 69 sisi tuliuza Pakistan na Pakistan nao waliweza kuuza kwetu bilioni 80.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa bahati mbaya hatuna ubalozi Pakistan. Balozi anayetumika anatoka India lakini na Waziri leo kasema kwamba kati ya India na Pakistan kumekuwa hakuna mahusiano mazuri ya kisiasa. Kwa hiyo, naomba sana Serikali kwamba iongeze, ifungue ubalozi Pakistan. Kenya na Uganda mwaka jana jumla wameuza dola milioni 154 biashara waliyoifanya na Pakistan. Kwa hiyo, kama tulivyofungua Indonesia tufungue na Pakistan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumekuwa na rafiki zetu wa damu katika nyakati mbalimbali, Iran ni mojawapo ya Taifa ambalo tumepita nalo katika nyakati mbalimbali kwa sera ya Mwalimu Nyerere alivyokuwa anatetea haki na unyanyasaji duniani kote. Iran limekuwa ni Taifa ambalo sisi tumesimama nalo katika nyakati mbalimbali, lakini kwa bahati mbaya Iran ni Taifa kubwa japo kama mtu halisemi, haliandiki lakini ukweli unabaki Iran ni Taifa kubwa hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuna Ubalozi Iran, tumefungua Ubalozi Israel, sitaki kusema kwamba kufungua Ubalozi Israel basi na Iran ufungue, lakini kwa umuhimu, kwa undugu wetu wa damu na Iran ni lazima tufungue ubalozi hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naiomba sana Serikali na Mheshimiwa Waziri jambo uliangalie na utumie kwamba sisi hatufungamani na upande wowote na Iran ni sehemu yetu muhimu kwa maana ya biashara na mahusiano yetu ya kindugu kama nilivyosema.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niseme kwenye economic diplomacy mambo makubwa yaliyofanyika kwamba ni biashara, sisi tunafanya biashara mbalimbali, tunatoa huduma kwa mfano Tanzania katika bandari yetu ile ni huduma, kuhudumia nchi ambazo hazina bandari.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba Serikali ijipange katika suala hili. Tumeichukua Congo katika East Africa na bahati nzuri sasa mizigo yetu mingi na nchi nyingine/wenzetu majirani walikuwa wanapata sasa imelekezwa kwetu. Lakini bado viko vikwazo vya kufanya biashara kwa maana ya kwamba kwenye mizani yetu kuna ucheleweshaji mkubwa, lakini na efficiency ya bandari yetu. Nilikuona naomba sana jambo hili Serikali iliangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nilitaka niongelee habari ya huduma ya matibabu. Nchi nyingi duniani na hata sisi wenyewe tumekuwa wakati mwingine tunaenda sana katika Taifa la India kwa ajili ya matibabu. Nataka nikwambie na nikupe taarifa kwamba Hospitali yetu ya Benjamin Mkapa sasa inapokea wagonjwa wengi kutoka nchi zinazotuzunguka hasa za Maziwa Makuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naomba Serikali itangaze kwa makusudi kwamba Benjamin Mkapa sasa ni center of excellency katika East and Central Africa, na tukifanya hivyo tuweke sasa huduma muhimu zinazopatikana kwenye suala la magonjwa kama ya figo, upasuaji na vitu vingine, sasa hospitali inafanya vizuri. (Makofi)

Kwa hiyo, nilikuwa naomba Waziri kupitia pamoja na Wizara ya Afya Hospitali ya Benjamin Mkapa ipewe vifaa vyote na huduma zote stahiki lakini tuitangaze kwamba kwa tangazo maalum sasa hii ni center ya excellency kwa East and Central Africa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka niongeze jambo la sisi kuteuliwa na SADC kwamba tuwe ni supplier wa dawa na ukiangalia kama Waziri alivyosema kumekuwa na wenzetu wanasuasua kutumia Tanzania kama sasa ndiyo procurement agency kwa ajili ya wao kupata dawa. Ni vyema Serikali ikawekeza kwamba badala ya sisi kuwa kama ni dalali basi tuwe na viwanda ili wenzetu wa SADC waweze kununua kwetu. (Makofi)

Kwa hiyo nilikuwa naomba sana na haileti logic kwamba mimi nikakununulie halafu nikuletee dawa kwa kuuzia. Ni bora tuweke viwanda vya kutosha hapa vya dawa ili waje wanunue kwetu badala ya sisi kuwa madalali kwa SADC.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mwisho kabisa, Mheshimiwa Waziri amesema habari ya kwamba sisi sasa ndiyo kitovu cha kupambana na ugaidi katika nchi za Kusini mwa Afrika (SADC). Habari hii ni njema lakini katika hisia si habari njema sana na sijui kwa nini Serikali walilichukua hivi na kutamka lile jambo lile nzito kwamba sisi tumekuwa excellency.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia kwenye bajeti ya Serikali. Nimepitia taarifa ya hali ya uchumi iliyowasilishwa na Mheshimiwa Waziri na kwa kweli nataka niipongeze Serikali kwa dhati, imepigana kwa nguvu zote kuhakikisha uchumi wetu upo katika hali nzuri. Fedha yetu imeimarika, lakini vilevile tumepambana na mfumuko wa bei kwa kiasi kikubwa. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali katika maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala zima la mfumuko wa bei na kuongezeka kwa pato la Taifa, Mheshimiwa Waziri ameongelea habari ya miradi yetu mikubwa tunayoendelea nayo. Kokote duniani construction industry inaleta matokeo makubwa zaidi katika kukua kwa pato la Taifa na hata ukipima GDP unaangalia na miradi ambayo inatekelezwa. Katika mchango wangu nataka nijikite kwenye namna gani viwanda vyetu vya ndani hasa viwanda vya simenti na niseme tu duniani kote Taifa ambalo linatumia simenti nyingi ni mataifa ambayo yana uchumi mkubwa. Katika Afrika Misri ndiyo inaongoza kwa matumizi makubwa ya simenti na hiyo vilevile hata GDP yao inaongezeka, lakini vilevile ni kipimo kwamba nchi hiyo ina uchumi mzuri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo na sisi katika suala zima la simenti hapa nchini, ni jambo la muhimu na lazima twende nalo hivyo hivyo. Shida iliyopo kwa sasa simenti yetu na bei yake imekuwa inaongezeka kila wakati badala ya kushuka. Kikubwa zaidi kinachotokea ni kwamba, lipo tatizo la malighafi inayoenda kutengeneza simenti na bahati mbaya viwanda vingi ambavyo vinatengeneza simenti vinanunua materials yale ya kutengeneza simenti kwa wafanyabiashara wadogo. Hakuna kampuni kubwa mahsusi ambayo inalisha viwanda hivi, lakini kibaya zaidi ipo Tume ya Madini ambayo inatoa bei elekezi za malighafi hizi ambazo zinalisha viwanda hivi.

Mheshimiwa Spika, mwezi Aprili mpaka mwezi Juni, Tume ya Madini imetoa bei elekezi za materials hizi ambazo zinatumika kutengeneza simenti. Kwa mfano, gypsum inauzwa kuanzia Sh.38,000 mpaka Sh.100,000. Sasa uchuke gypsum kutoka Itigi uipeleke Tanga kwa ajili ya simenti, uipeleke Mtwara au uipeleke Dar es Salaam lakini bei ya tani moja kuisafirisha ni Sh.123, bei iliyopo sasa hivi katika transport. Kwa hiyo unakuta hakuna mtu ambaye anataka kuwekeza katika biashara hii.

Mheshimiwa Spika, naomba ku-declare interest nafanya kazi ya ku-supply feldspar katika kiwanda mojawapo kinachotengeneza tiles. Bei hiyo ambayo tunapangiwa na Tume ya Madini inatuumiza kwa kiasi kikubwa. Kwa hiyo huwezi ukaingiza mtaji wako mkubwa uwe na magari ya kusafirisha, kazi iliyofanyika wafanyabiashara weni wanadaka gari kwenye barabara hizi Msamvu pale, wanadaka gari maeneo mbalimbali, hakuna kampuni mahsusi. Kwa hiyo Waziri katika hotuba yake ukienda katika ukurasa wa 10 amegusia habari ya kuondoa mrabaha katika makaa ya mawe na anasema ni Sura 123 ya Sheria ya Madini, kwamba kupunguza kiwango cha mrabaha kutoka kwenye makaa mawe yanayotumika kama malighafi ya kuzalisha nishati viwandani kutoka 3% hadi 1%. Lengo la hatua hii ni kupunguza gharama za uzalishaji viwandani, kuchochea uwekezaji zaidi na kukuza ajira.

Mheshimiwa Spika, jambo hili ni jema, lakini naomba Serikali iondoe malighafi kwenye viwanda ambavyo vinazalisha simenti na kama hili nililosema kwenye tiles na watoe kodi tunayolipa ya VAT kwa sababu VAT tena inakuja kulipwa kwenye kiwanda baada ya kuuza zile bidhaa, lakini kufanya hivyo unachochea supply ya materials kwenye viwanda kuwa kubwa. Kufanya hivyo italeta ahueni kwa wafanyabiashara wanao-supply kule kwenye viwanda lakini vilevile na kupunguza bei ya simenti.

Mheshimiwa Spika, ukienda katika Sheria ya Madini, Sura 123, kwenye regulations za mwaka 2019 wameongelea habari ya kuondoa kodi kwenye baadhi ya madini, lakini kwa makusudi kabisa sheria inasema sheria hii haihusishi, that trading of building all industrial energy minerals shall not apply to these regulations. Kwa hiyo naiomba sana Serikali na Mheshimiwa Waziri aangalie jinsi ya kuondoa kodi kwenye malighafi hizi na kufanya hivyo kutachochea kwa kiasi kikubwa kwamba viwanda vyetu hasahasa vya ujenzi viweze kupata malighafi na hivyo kuweza kushusha bei ya simenti hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kwenye suala lingine kuhusu Shirika la Bima la Taifa. Kama unavyojua biashara ya bima imekua hapa nchini, lakini na sisi tuna Shirika la Bima la Taifa. Bahati mbaya shirika hili bado linaendeshwa katika muktadha wa Kiserikali, nataka niishauri Serikali iajiri watu ambao wanaenda kufanya biashara ya bima, lakini vilevile walipe fedha shirika hili. Tunavyojua kwamba Serikali haiyawekei bima magari yake, lakini zipo taasisi ambazo zinafanya biashara nazo zipo exempted kwenye bima. Ninachotaka kusema ni kuwa, si kwamba hili Shirika la Bima la Taifa wapendelewe na Serikali, hapana lakini wawezeshwe ili waweze kufanya biashara kama kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nije kwenye suala la kubadilisha matumizi ya Ranch ya Kongwa sasa ianze kulima alizeti na unaweza kukuta si tu alizeti na watataka walime na mahindi na vitu vingine. Mimi napinga jambo hili kwa kiasi kikubwa. Nimesoma kwenye hotuba ya Waziri katika sehemu ya masuala ya mifugo kwenye importation ya product kutoka nje na Waziri alisema kwamba nyama yetu bado haina ubora, lakini kinachotuzuia ni kwamba hatujaamua kama Serikali kuwekeza katika suala zima la kutoa nyama zenye ubora.

Mheshimiwa Spika, Ranch ile ya Kongwa ina capacity kwa sasa ya kuwa na ng’ombe 11,400, lakini na hiyo tumetoa nusu tumewapa baadhi ya wananchi wanachunga mle, vijiji vinavyozunguka, lakini ukija katika capacity yake nzima ina uwezo wakuwa na ng’ombe 40,000 kwa wakati mmoja. Nataka niseme Serikali iliangalie jambo hili, yapo mapori mengi wasikimbilie kupeleka alizeti sehemu ambayo haihusiki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa Unaokusudia Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa dhati kabisa kwa kunipa nafasi niweze kuchangia Mpango huu wa Maendeleo. Awali ya yote nimpongeze Waziri wa Mipango pamoja na Waziri wa Fedha kwa kutuletea Mpango huu ambao kwa kiasi kikubwa inaonyesha namna gani ya kutekeleza na kuleta maendeleo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja katika watu ambao nilichangia katika Bunge lililopita mwaka jana ilikuwa ni kwamba tuwe na Tume ya Mipango. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa kuamua kwa dhati kabisa tuwe na Tume ya Mipango, lakini dhana na dhima ya Tume ya Mipango ni kuwa na dira kubwa na kuangalia namna gani Taifa tunalotaka kwenda katika vipaumbele vyetu na katika kujiimarisha zaidi kiuchumi. Nataka nimshauri Waziri wa Mipango, kwamba sera zetu zijielekeze katika kutatua matatizo na kuyamaliza badala ya kuwa na sera za jumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwa Mkoa wa Dodoma, tunaishukuru Serikali sasa ni Makao Makuu ya Nchi, kazi tuliyonayo ni kwamba tunajenga Mji huu, lakini ukiangalia kwa sasa Dodoma haina viwanda umebaki Mji wa Kiserikali, umebaki mji ambapo mzunguko wake wa fedha sio mkubwa kwa sababu hatuna viwanda, Umebaki ni mji wa mwisho wa mwezi, ikifika mwisho wa mwezi mzunguko wa fedha unakuwa mkubwa na tarehe zinavyoisha, unaona kabisa uchumi na watu hawajachangamka. Kwa hiyo, ni lazima tuwe na viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa Dodoma huoni bidhaa zinazotoka Dodoma ziende Iringa, Arusha, Kanda ya Ziwa, bado tuna shida ya viwanda. Kwa hiyo, Dodoma inahitaji sera madhubuti kwa namna gani iwe hub…

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana ya kuwa na uchumi wa kuweza kuzalisha katika ili kuhudumia mikoa mingine …

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Ni wapi inatajwa taarifa?

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi hapa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kenneth Nollo, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Hamisi Taletale.



TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji, hapa Dodoma mnacho Kiwanda cha Wine au hicho sio Kiwanda? Ni hayo tu.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kenneth Nollo, unaipokea taarifa hiyo.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa kutoka kwa Ustadhi, kwa kujua hili suala la wine, naipokea taarifa ni kweli kiwanda tunacho na kwenye hili bado tuna changamoto, lakini tunaendelea kuweka jitihada zaidi kukuza zao la zabibu. Nakushukuru sana Ndugu yangu Mheshimiwa Taletale. Nilichotaka kusema ni kwamba mji huu unahitaji uwe na viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka niliseme hususani kwa Mkoa wa Dodoma, Waziri amesema habari ya kwamba umaskini unaenda kupungua, lakini kwa Mkoa wa Dodoma, bado kuna shida. Nature yetu ni kwamba Mkoa wetu una ukame, hilo wote tukubaliane, kwamba Mkoa wetu na maeneo yetu ya Kanda ya Kati, ni maeneo kame na umaskini bado ni mkubwa kwa sababu moja, wananchi wengi wanategemea kilimo, lakini jitihada za kuondoa umaskini kwenye suala zima la kilimo na kama nilivyosema namna ya kuweka viwanda, bado hatujakaa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwa na Sera za Kitaifa, Mipango ya Kitaifa, wenzetu kwa mfano Nchi ya Nigeria walikuwa na sera kwa ajili ya maeneo kame, mipango kwa ajili ya maeneo kame. Naishauri Serikali na namshauri Waziri wa Mipango, tuwe na sera mahsusi katika kuinua na kuleta uchumi kwenye maeneo kame ikiwemo Dodoma. Sawa tunapokea skills za umwagiliaji, lakini bado haitoshi, wananchi wengi wa maeneo yetu kwanza idadi ya watu inaongezeka, ardhi ya kulima inapungua ni lazima Serikali iangalie uchumi wa maeneo haya kame tunafanya nini, hili nataka niliongeze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine kuhusu wanafunzi wanaosoma Vyuo Vikuu na Vyuo vya Juu. Kutokana na umaskini tulionao kwenye maeneo yetu hasa Kanda ya Kati, watoto wengi hawawezi kwenda kwenye vyuo wakalipiwa ada kwa sababu uwezo wa wazazi wao haukidhi. Nalisema hili kama Mbunge, changamoto ninazozipata kwa sasa, kila mtoto ameshindwa kwenda shule na wanasema Mbunge tusaidie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kama inaweza kwa nini tusiondoe ada kwenye Vyuo Vikuu tukopeshe watoto kwa ajili ya chakula, fedha ya chakula. Serikali itoe ada kwenye Vyuo Vikuu kwa watoto wa Kitanzania ila kama ni foreign students hao ndiyo walipe ada. Nataka niulize Serikali inapata faida gani kulipisha watu wake kwenye ada za Chuo Kikuu? Naomba sana jambo hili tulitafakari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umaskini ni mkubwa, watoto wetu hawawezi kwenda vyuo na wengi wanaacha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)