Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Tarimba Gulam Abbas (25 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii, maana nilishakata tamaa, nilijua leo sipati nafasi. Namshukuru Mwenyezi Mungu Subhana-huwataala kwa kutuwezesha kuwepo hapa. Nakishukuru chama changu kwa kunipeleka mbele ya wananchi wa Kinondoni na hatimaye wakanichagua kwa kura nyingi sana. Nawaambia wananchi wa Kinondoni niko imara, nina nguvu, nina akili ya kuwatumikia kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naishukuru familia yangu ikiongozwa na mke wangu Latifa Hasnal Faizal na dada yangu kipenzi Zera Abbas Muhammad Ali ambao kwa kipindi chote wamekuwa ni silaha kubwa katika kuniwezesha kusimama nikawa imara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Hotuba ya Mheshimiwa Rais aliyoitoa wakati akizindua Bunge hili la Kumi na Mbili, yenyewe inatosha kuwa ni dira ya vipaumbele kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu hili kwa kipindi cha miaka mitano inayokuja. Hata wataalam wa mipango wanaweza wakafyonza humo ndani na wakapata vitu ambavyo Watanzania wengine watavipokea kwa mikono miwili. Siyo rahisi kuandika hotuba kama ile, Rais lazima atakuwa ni mtu mwadilifu, ambaye amemweka Mungu mbele kuangalia Watanzania wanahitaji nini, awafanyie nini na nchi yake iko wapi na anataka aione iko wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, huyu ni mtu ambaye anaongozwa na hofu ya Mungu. Hii inanifanya niseme kwamba viongozi wa Serikali wawe ni wateuliwa Mikoani au Wilayani, Serikali Kuu wawe na hofu ya Mwenyezi Mungu katika kufanya kazi zao. Hapo tutafanikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba uniruhusu nisome maneno ya Mwenyezi Mungu ambayo ameyasema. Aliwauliza binadamu lakini akajibu mwenyewe; iko katika Surat Azuma aya ya 9, nitaisoma kama ilivyo, anasema: “Hal astawi? (Anauliza, wanafanana?) Aladhina yaalamuna waladhina laayaalamuna. (Yule anayeijua na yule ambaye hajui, hawa watu wamoja wanafanana hawa?) Akajibu, Mwenyezi Mungu hakusubiri watu wamjibu, akasema, balaa (hapana).” Maana yake imekusudiwa mtu mwenye hofu ya Mwenyezi Mungu ni mtu ambaye amepata daraja kubwa sana mbele ya Mwenyezi Mungu. Tushukuru kwamba tuna Rais ambaye ana hofu ya Mwenyezi Mungu na ndiyo maana mipangoyake inakubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu zangu, sisi Wabunge wote humu tumekuja hapa kwa niaba ya wananchi wa Tanzania, tunapozungumza humu ndani hatuzungumzi kwa utashi wetu, ni utashi wa wananchi waliotutuma. Wananchi wakitueleza kwamba nendeni Bungeni kazungumzieni suala fulani, kaiambieni Serikali yetu suala fulani, Serikali ni ya wananchi na Bunge ni la wananchi, wapi tunakinzana? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii kila Mbunge akisimama anaongelea kuhusu TARURA; Spika anazungumzia TARURA, kila mtu anazungumzia TARURA, jamani sasa ifike wakati Serikali msikie hili. Huo ndiyo uadilifu ninaouzungumza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wengi humu ndani tukizungumza, maana yake ni kauli ya Mungu, ni kauli ya wananchi na hapo ndipo tutapata mafanikio. Kuna options nyingi tu ambazo zimewahi kujadiliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama TANROADS hatuwezi tukapunguza fedha zake, iunganisheni na TARURA iwe ni kama division ya TARURA, wawe na mfuko mmoja mkubwa, wafanye kazi pamoja. Siyo lazima tuwe na utitiri wa vyombo, hapana, vyombo vinaweza vikawa vichache, kazi zikawa kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Magufuli is alone, anasaidiwa na watu wachache lakini anafanya kazi kubwa, it is possible! Kwa nini hatumuigi Mheshimiwa Rais? Mbona kaitembelea Tanzania nzima? Wote humu ndani tumepata fadhila zake, tumetumia jina la Mheshimiwa Magufuli katika kupita. Aljazaul-ihisani ilal-ihisani (Anayekufanyia wema, mrudishie wema). Mheshimiwa Dkt. Magufuli katufanyia wema mkubwa katika Taifa hili. Tumrudishieni basi wema kwa kuwatumikia wananchi wake. (Makofi)

(Hapa kengele iligonga kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nisije siku nyingine nikaomba habari za Kinondoni Waheshimiwa mkanikatalia, lakini nataka…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa kengele imeshagonga. Ahsante sana.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Basi nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ni mmoja kati ya Wajumbe wa Kamati ya Bajeti. Nimepata nafasi nzuri sana ya kuupitia Mpango huu. Nimeuona, tumeujadili, nasema ni Mpango mzuri ambao Serikali imekuja nao, lakini naiomba Serikali iweke room for improvement. Haya maoni ambayo yanatolewa yote ni maoni mazuri, wayachukue, isiwe kama ni taratibu zile nyingine kwamba tunazungumza lakini bado wanakuja na Mpango ule ule, mapendekezo yale yale, hilo haitakuwa jambo jema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najikita zaidi katika private sector. Ningependa sana huu Mpango uje waziwazi kwenye private sector, tuwe na vibrant private sector, hakuna uchumi unaoweza ukaendelea bila ya kuwa na private sector ambayo ina nguvu, inayochochea exports, lakini vile vile inachochea domestic spending, bila mambo haya tutakuwa tunajidanganya. Tutakuwa tunazungumza lakini tunajifanya kama tunasahau kama private sector ni mbia mkubwa sana wa maendeleo katika nchi yetu. Tumeangalia na figure zimetolewa na Wizara. Tuchukue tu mfano wa ule Mpango ambao umemalizika 2021. Contribution ya private sector ilikuwa inatarajiwa trilioni 48 karibu asilimia 45 ya kile kinachotarajiwa. Huyu si mtu wa kawaida. Huyu ni mbia ambaye lazima tuhakikishe tunakuwa nae na tunamuamini, private sector lazima iaminiwe. Tusitengeneze private sector ambayo hatma yake tunapeleka wrong waives, wrong information or wrong message kwa investors nje kwamba kufanya kazi au biashara Tanzania ni jambo gumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni wazi, hebu angalia hawa wataalam wa World Bank, kuna huyu mtaalam anaitwa Simeon Diankov na Gerald Paul, Wachumi wa World Bank hawa walivyotengeneza ile ease of doing business index, Tanzania katika kuangaliwa, tuko watu wa 141, tumewekwa kama medium. Sasa jamani tunashindwa, Rwanda is very easy to do business, Rwanda jamani? Kitu gani kinatufanya Rwanda wao iwe ni easy to do business, sisi iwe ni medium, basi hata Zambia? Zambia nao wanafanya vizuri, wako easy, Kenya wako easy, sisi tunafunga wapi kiasi kwamba kwetu sisi ionekane tuko katikati, tunachotafuta ni nini? Tunatafuta industry ya private iwe inapewa nafasi zake. Sasa hivi iko suffocated, it is a fact, nimepata bahati ya kufanya kazi Serikalini, nimefanya kazi katika Private Sector, sasa hivi na mimi eti nami ni mwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sikiliza, kampuni moja inazungukwa na regulators si chini ya sita au saba. Huyu anamuuliza hiki, yule anamuuliza hiki, yule anamuuliza hiki. Hajui aende wapi, who is the core regulator, aende wapi. Akipata matatizo, akiwa aggrieved huyu mtu anapata shida kubwa sana. Kampuni zinapata shida kubwa sana na haya ambayo yalikuwa yakizungumzwa kwamba business zinafungwa, naomba Serikali iangalie. Haiwezekani kampuni moja itaangaliwa na TRA, BOT, TCRA, OSHA, Fair Competition and Filling Company, hiyo ni mfano wa kwenye betting, huko usifikiri kuna Gaming Board of Tanzania peke yake, hawa ninaowatajia wako nyuma kila siku wanagonga milango. How can you do business?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunachohitaji ni kuona kwamba mtu ambaye anafanya business Tanzania asababishe mwingine aliye nje avutike kuja Tanzania. Kwa kufanya hivyo tutapata kodi nyingi, tutaajiri watu wengi, lakini vile vile tutaondoa manung’uniko. Leo hii mtu akiwa aggrieved anakwenda wapi? Kwa nini tusiwe na regulatory ombudsman? Wafanyabiashara hawataki kwenda Mahakamani kushindana na Serikali. Katika vitu ambavyo wafanyabiashara hataki ni ugomvi na Serikali, lakini angekuwepo mtu hapo kama vile wa tax ombudsman hata regulatory ombudsman amekuwa aggrieved na chombo fulani cha Serikali huyu bwana anakwenda kwa ombudsman, anakwenda pale anazungumza mambo yake yanawekwa sawa, mambo yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tutaendelea na utaratibu tulionao sasa hivi, tuna suffocate private sector na private sector kama nilivyosema awali ni eneo moja ambalo ni mbia mkubwa sana wa biashara, mbia mkubwa wa maendeleo na ni maeneo ambayo tunahitaji kuyaangalia kwa nguvu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. Mungu atubariki. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ili niweze kuchangia hoja ambayo Yanga mwenzangu ameileta ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa kwa miaka mitano hadi mwaka 2025/ 2026.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda kuunga mkono hoja hii na nina sababu kadhaa za kuunga mkono na wakati huohuo kuleta mapendekezo ambayo naamini kabisa kwa namna moja au nyingine yataweza kuboresha Mpango huu ambao leo tunaujadili. Nitaanza na hii dhana ya Serikali Sikivu. Mpango wowote ambao Serikali inaubuni ni lazima isikilize maoni kutoka kwa wachangiaji, hasa kutoka kwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, Serikali Sikivi imeoneshwa vizuri sana na Mheshimiwa Rais Samia naamini kwa kusikiliza mchango tuliokuwa tunautoa mwezi wa pili. Tulizungumza kuhusu ufanyaji kazi wa TRA na jinsi gani TRA inavyotukosesha mapato pale ambapo taratibu za ukusanyaji wa mapato zinavyokuwa sio sahihi. Vilevile tukazungumza suala la baadhi ya biashara kufungwa kutokana na ugumu wa ufanyaji kazi, Mheshimiwa Rais alichukua hatua za haraka sana. Naomba tumpongeze Mheshimiwa Samia kwa kusikiliza, hii ndiyo maana thabiti kabisa unapozungumzia Serikali Sikivu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali imeonesha mwelekeo mpya huko nje business community imekuwa na imani kubwa sana na Serikali. Nina imani kabisa kutokana na imani ambayo inajengwa sasa wasaidizi wa Mheshimiwa Rais akiwemo ndugu yangu Mheshimiwa Mwigulu Mchemba atasikiliza vizuri hoja zetu ambazo tunazileta uzichuje, zisaidie huu Mpango ili uwe bora zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye suala zima la maendeleo, nataka nimuangalie Mheshimiwa Hayati Julius Nyerere ambaye aliwahi kuzungumza na akatoa kauli ni nini maana ya maendeleo. Hili limekuwa likizungumzwa pia na Waheshimiwa Wabunge katika Mabunge mengi yaliyopita.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hayati Nyerere anasema: “Maendeleo hayawezi yakawa maendeleo kama sio people centred.” Maendeleo lazima yaguse watu ndipo yatakuwa ni maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haina maana vitu sio sehemu ya maendeleo, hapana, vitu ni sehemu ya maendeleo, lakini lazima i-translate na ishuke chini kwa mwananchi mmoja- mmoja. Hapo ndipo panapotuletea maelezo ama swali, je, Mpango huu unamgusa vipi mwananchi wa kawaida? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani tuangalie hapo kwamba, Mpango huu lazima uwe na vielelezo vinavyopelekea mwananchi wa kawaida kusema naam, Serikali inakuja na mpango ambao utanigusa mimi, yule na mwisho jumuiya nzima ya Watanzania watafaidika na mpango huu. Yote haya ambayo tunayasema yanaelekea katika maeneo mazima ya uhuru wa watu kuweza kufanya biashara zao, kufanya kilimo chao katika nchi yao, kupata mazao ambayo wanaweza wakayapeleka nje wakaenda kuyauza. Hata utawala wa kisheria kwa sababu, kuna wakati tulilalamika sana hapa yale ambayo yanapangwa katika sheria nayo hayatekelezwi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulikuwepo na mjadala mkubwa sana, sitaki nirudie huko, mjadala ambao ndugu yangu msemaji wa mwisho alizungumzia wa korosho ule uliumiza watu wengi sana. Turudi katika utawala ule ambao tumejiwekea sheria zetu na zile sheria tuzifuate. Naamini kwa muelekeo ambao umeoneshwa na Mheshimiwa Rais ni dhahiri kabisa haya sasa yanakwenda kutekelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia Serikali imezungumza mambo mengi sana humu ndani, lakini Mpango huu lazima uwe ni unaotekelezeka. Tunataka Serikali itakavyokuja kufanya majumuisho itueleze ni namna gani imejitayarisha kuhakikisha kwamba inaitumia sekta binafsi ambayo ndiyo itakuwa ni moja kati ya wabia wakubwa katika Mpango huu. Ukiangalia numbers zinaonesha shilingi trilioni 40.6 zitatoka katika mchango wa sekta binafsi, lakini hata ule mchango wa Serikali wa shilingi trilioni 74.2 mchango ule utatetegemea vilevile sekta binafsi, Serikali haifanyi biashara. Ili 74.2 trillion shillings ziweze kukusanywa lazima business community hapa sasa iweze kuangaliwa na kuwa natured vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hali hiyo, napenda nione kwamba, mchango wa Serikali katika kuhakikisha kwamba business community inalelewa vizuri uweze kuelekeza vizuri zaidi na Mheshimiwa Waziri aje kutuambia maana kuna kitu kimoja mimi kimenitia moyo, lakini kimenisononesha. Tuna watu wazuri sana katika nchi hii katika mawazo mema ya kufanya biashara na hapa nimpongeze Mpinzani wangu Mohamed Dewji ambaye tumesikia ameteuliwa na Rais wa South Africa kuwa ni mmoja kati ya watu ambao watamshauri. Sasa kama tuna mtu kama yule ndani ya Tanzania ambaye wenzetu wanamuona, sisi tunawatumiaje watu kama hawa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ndipo sasa naiomba Serikali na napendekeza kwamba ni wakati umefika sasa Serikali ikaunda angalau timu ya wataalamu pamoja na wafanyabiashara mashuhuri, wakiwemo watu kama Mohamed Dewji, watueleze tufanyeje ili tuweze kufanikiwa zaidi katika suala zima la uwekezaji katika nchi yetu. Tuangalie tu, tusemeni kweli, Kamati ya Bajeti inazungumzia kwamba haijaridhika kuona kwamba Tanzania ni nchi ambayo si nyepesi ya kufanya biashara na wakatoa numbers wakasema tuko nafasi ya 141. Hata Mpango ule unaomalizika sasa ulikuwa unajitahidi kuifanya Tanzania iwe ndani ya nchi 100 katika wepesi wa kufanya biashara, lakini hatukufika huko. Ni vikwazo gani vilivyosababisha Tanzania isiweze kuingia katika zile nchi 100 zenye wepesi wa kufanya biashara? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa Serikali itakapokuja Mheshimiwa Dkt. Mwigulu atueleze ni vitu gani ambavyo watavifanya kuhakikisha Tanzania inakuwa ni moja kati ya nchi ambazo ni easy to do business, ili wawekezaji waweze kuvutika na wakaja. Kwa sababu bila wawekezaji ukweli ni kwamba tutapata maendeleo, lakini yatachelewa na tusingependa kuchelewa. Mkumbuke Rais wetu aliyepita, Hayati Mheshimiwa Magufuli, aliisababisha Tanzania kwa haraka zaidi kuingia katika Uchumi wa Chini wa Kati, miaka mitano kabla. Naamini kabisa Mheshimiwa Suluhu Hassan atatusogeza mbele zaidi ya pale ambapo Mheshimiwa Hayati Magufuli ameacha, kama mipango hii mizuri ambayo imewekwa itaweza kutekelezwa na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho napenda nizungumzie kuhusu ahadi za viongozi wetu wakuu. Wananchi wana imani sana na Serikali, wana imani sana na viongozi wao wakuu. Leo hii Wabunge tumekuwa tukilalamika sana tunazungumzia barabara za miaka mitatu, minne, mitano ambazo Mheshimiwa Rais alitoa ahadi. Sasa tusiende mahali tukafikia kwamba viongozi wetu wakitoa ahadi wananchi wa kawaida waseme, aah, haya ni kama yale yaliyopita, lazima tuyaangalie.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu nampenda sana, kwa hiyo, napenda nione safari hii tunabadilisha mwelekeo, viongozi wakuu wakitoa ahadi zao wasaidizi wake wawe ni hodari wa kuzipokea na kuzifanyia kazi. Hatutataka tuje tukumbushie miaka mitatu iliyopita. Mheshimiwa Rais kama anayasikia haya nitaomba awape support ya kutosha Mawaziri wake katika suala kama hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemaliza na nilisema naunga mkono hoja hii, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nivunje utaratibu kidogo, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Ameir Mohammed, kwa uamuzi wake wa busara, kwa leo kutamka ndani ya Bunge lako tukufu, kwamba anakuwa mwananchi na hii ifungue milango kwa waheshimiwa wabunge wengine waweze kufuata mfano mzuri kama huu na namuombea Mwenyezi Mungu majaze busara zaidi Mheshimiwa Ameir Mohammed. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo...

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Taarifa Mwenyekiti.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Rashid Shangazi.

T A A R I F A

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayezungumza hapa ndio Mwenyekiti wa wabunge wa Simba hapa mjengoni, na katika makabrasha yetu hatujawahi kuwa na mwanachama anayeitwa Ameir Abdalla Ameir, ahsante. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tarimba taarifa unaipokea.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ananipotezea muda na naomba uulinde muda wangu ndio kwanza naanza, sasa ndio naanza. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi ambayo nitaitumia vizuri, katika kuhakikisha nachangia vizuri katika hotuba hii ya Mheshimiwa Dkt. Mwigulu. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, na ninaweza kusema katika historia ya hotuba za bajeti, hotuba ambayo imewagusa wananchi kwa kiasi kikubwa sana ni hotuba hii, imejaa ubunifu na inanipelekea nimuombe Mwenyezi Mungu amjaalie Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan, yeye na timu yake. Mawaziri hawa wakiwemo ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na wengine wote wanaomsaidia, Mwenyezi Mungu awajaalie afya, uzima na akili nyingi sana za kuwa wabunifu kama walivyofanya safari hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitachangia katika eneo moja, na eneo lenyewe ni sera na mikakati ya kuongeza mapato na kama ilivyo katika Ibara ya 25 ya hotuba, kwa wale ambao wanacho hicho kitabu naomba wapeleke hapo macho yao. Na nikipata muda nitagusia jimboni kwangu Kinondoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaenda kuchangia nawaombeni siku ya Jumanne, wabunge wote tuwemo ndani ya Bunge hili tuipigie kura ya ndio bajeti hii. Kama alivyosema ndugu yangu Mheshimiwa Shangazi kwamba Wabunge wote wawemo ndani ya ukumbi, siku ya Jumanne basi Mwenyezi Mungu awajaalie wote wawepo humu ndani, ili bajeti hii ipate kupigiwa kura ya ndio pamoja na wenzetu walio upande ule kule walio wachache. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najaribu kusoma azma ya Serikali ya kuboresha mazingira ya kufanya biashara kwa kuweka mazingira rafiki kwa mlipa kodi, ili wawavutie wawekezaji na vile vile kundi la wafanyabiashara wadogo na wakati, ili waweze kupanua wigo wa kodi ni jambo zuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naisoma hii pamoja na ile azma nyengine ya kujenga uchimu shindani wa viwanda kwa maeneleo ya watu. Haya ni madhima mawili makubwa sana ambayo Serikali lazima iangalie kwa macho ya uangavu kabisa. Kwa sabau gani, kwa sababu hivi vitu vinakinzana na hali ya sheria zilizopo nchini pamoja na sheria za kodi hazionekani kabisa kuipa support hiyo azma ya Serikali ya kujenga uchumi shindani na viwanda kwa ajili ya maendeo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka niwape mifano miwili mikubwa kabisa, na hii inahusu watanzania ambao wamejaribu kujenga viwanda vya madawa hapa Tanzania, changamoto zao wanazozipata ukilinganisha na dawa zile ambazo zinazotengenezwa nje na kuletwa nchini, sasa hivi hapa Tanzania dawa ambazo tunazitegemea sana ni dawa zinazotoka nje, na kulifanyika utafiti August mwaka 2019, yupo bwana Dikson Pius Wande na wenzake, walifanya utafiti juu ya mahitaji ya dawa katika nchi hii, na wakaona kwamba katika mwaka 2021, dawa ambazo zinakwenda kuingizwa Tanzania ni karibu zenye dhamani ya dola milioni 906, sawa na katibu trilioni 2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hali hiyo utakuta hizi ni dawa zinazoletwa na private sector peke yake, achilia zile dawa ambazo zinaletwa na Serikali. Sasa ukiangalia utakuta kwamba wanaojenga viwanda vya madawa nchini, wao wanapata misukosuko mikubwa sana kwa kuwa hali ya sheria za kodi haimpi nafuu mjengaji wa viawanda vya madawa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii utashangaa cough syrup, juzi nimenunua cough syrup kutoka Bangladesh shilingi 3,000 lakini cough syrup hiyo hiyo, ya in gradients hizo hizo ya Tanzania ni zaidi ya shilingi 3,000. Kwa kuwa tuna kasumba ya kuona kwamba dawa za nje ndio nzuri tunakimbilia kununua zile ambazo ni nafuu vile vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikwambie kitu kimoja, kwamba watafiti wale wanasema, katika mwaka mmoja unaokuja mahitaji ya dawa yataongezeka kwa asilima 28, maanda yake tunawasaidia wenye viwanda vya nje na wafanya biashara wa nje, kuendelea kuvuna fedha za Tanzania, wakati Tanzania tunaweza kutoa tukatoa unafuu mkubwa kwa wajengaji wetu wa viwanda, ili hata ile azma ya Serikali inayosema kwamba watu wajenge Tanzania ya viwanda iweze kutimia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo mtu ambaye anatengeneza cough syrup Tanzania, pengine atahitaji kuleta zile chupa, angalia hapo akileta ile chupa anaambiwa lazima aweke na label moja kwa moja huko inakotoka, label zenyewe ni za karatasi, zikija hapa zinaingiwa katika mifumo ya kusafisha chupa zile, lebo zinaharibika, na wanaambiwa hivyo ili wapate msamaha wa VAT lazima watimize masharti kama hayo, sasa masharti gani hayo, tuweke masharti ambayo yataidia viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri Mheshimiwa Dkt. Mwigulu yupo katika Serikali ambayo ni Sikivu, na wewe bahati nzuri Mwenyezi mungu amekujaalia kuwa mwananchi, na wananchi ni wasikivu. Hebu sikiliza kilio cha wananchi ambao wanajenga viwanda Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba twende sehemu nyengine, katika masuala yanayohusiana na unafuu wa kufanya biashara, wafanya biashara hasa upande wa TRA. Hebu angalieni dispute resolution ya makodi haya, Kamishna anapoandikiwa kwenye dispute resolution kama ilivyo kwenye sheria ya TAA katika part 7, utakuta kwamba kuna mlolongo mkubwa sana wa kuondoa haya matatizo ambayo yanatokana na decisions zinazofanywa na Kamishna, na zenyewe zinasababisha mashauri yazidi kule kwenye tax board appeal inafanya tukose kupata fedha za Serikali kwa sababu mashauri hayaendi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningekuomba katika hili Serikali ifanye utafiti iweze ikaangalia sheria zile kinzani ambazo hazitupi manufaa katika sera yetu ya Tanzania ya viwanda uzifanyie marekebisho, na hazi ni sheria zote mifumo ya licenses, mifumo ya usimamizi na mifumo ya kodi inahitaji kuangaliwa vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa niende Kinondoni. Nataka niseme kwamba bajeti hii imetufanyia kazi kubwa sana, na namshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuweza kuja na bajeti ambayo wabunge wengi wameisifia, hasa upande pale tulivyopewa shilingi milioni 500 kwa kila Jimbo. Nataka niwaambie milioni 500 kwangu hazitajenga lami lakini kuna barabara nyingi ambazo nitakwenda kuzitengeneza kwa kiwango cha changarawe, ili ziweze kupitika. Wananchi wa Kinondoni wanaonisikiliza, barabara ya Wibu, barabara ya Ufipa, barabara ya Chogo, barabara ya Wakulima, barabara ya Gulwe, Mkalama, Lalago, Sekenke, Mkunguni, Kiwanjani, Mapera kote huko tunakwenda kuzijenga hizi, angalieni bajeti ya wananchi inavyo kwenda ufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupongeze wewe pamoja na Serikali, kwa kuliona suala la kulitengeneza mto Msimbazi ambao ni kero kubwa sana, Dar es Salaam, na nataka niwambie kwa kutengeneza mto msimbazi sio tu Kinondoni inakwenda kufaidika Dar es Salaam nzima inakwenda kufaidika, kwa sababu mto Msimbazi ukifurika magari hayapiti Morogoro road, sasa hivi magari yatakuwa na nafasi ya kwenda kupita, daraja itajengwa, wananchi wa Kigogo, Mzimuni, Magomeni wote wanakwenda kupata nafuu ya jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni fedha nyingi sana ambazo Serikali imeziweka, kutokana na hili nataka niwaambie wananchi wa Kinondoni kwamba wamuombee Mheshimiwa Rais, wamuombee Mheshimiwa Waziri Dkt. Mwiguli pamoja na Serikali nziama, kwa sababu tayari..

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante!

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, aaah! Unanitoa raha lakini nikushukuru sana na naunge mkono hoja hii, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kipee wewe mwenyewe binafsi, kwa kunipa nafasi hii lakini nitumie nafasi hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wanamichezo kwa heshima kubwa walionipa ya kunichagua kuwa Mwenyekiti wa Bunge Sports Club tena katika uchaguzi ambao kwa bahati mbaya sana sikuwepo, hivyo nilichaguliwa nikiwa sipo nataka niwaambie kwamba nitarudishia hisani hiyo kwa kuwatumikia kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mchango wangu naupeleka kwenye masuala ya barabara, nimekuwa nikiangalia kila Mheshimiwa Mbunge anayesimama karibu asilimia zaidi ya 80 ya sisi tuliomo humu ndani tumekuwa tukizungumzia suala la TARURA. TARURA ni chombo kipya chombo ambacho tumekipa majukumu makubwa sana zaidi ya mzigo wanaoweza kuubeba. Wenyewe hawana chanzo cha fedha zaidi ya allocation ambayo Serikali inawapa kupitia road fund.

Mheshimiwa Spika, wanamtandao wa zaidi ya kilomita laki 100 na katika hizo kilomita zaidi ya 78,000 zote ni mbaya, unategemea nini katika utaratibu tunaotaka kwenda nao wa kuinua tija na kuinua mapato kwa wananchi wetu kuinua uchumi katika nchi ambayo barabara nyingi kwa mujibu wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri ni barabara mbaya unapata wapi tija na uchumi ukakuwa kwa kasi tunayoitaka si rahisi.

Mheshimiwa Spika, na ubaya utakuta kwamba TARURA yenyewe kwa kuwa ipoipo natumia neno ipoipo kwasababu haijakuwa intergrated na mifumo ya kisheria iliyopo katika nchi hii. Nawapa mfano mmoja ukiangalia sheria ya Urban Planning Act ile ya mwaka 2007, hasa section seven ambayo inatoa mamlaka ya upangaji wa miji, kwa mamlaka za city, municipal, ama za mjini. Lakini TARURA inakuja inafanya maamuzi yake ya kujenga barabara vile wanavyotaka wao hakuna consultation kati ya TARURA na urban authorities ama planning authorities na hiyo inatupa matatizo makubwa kwasababu user ni wananchi wa maeneo husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano pale Kinondoni, utakuta kwamba Kinondoni tuko mjini lakini ukienda kwenye kata zote hali ni mbaya sana katika sana katika barabara. Ukienda Kigogo hali mbaya, ukienda Mwananyamala angalau kidogo ukienda Makumbusho ukienda wapi unamleta Manager wa TARURA kwa mfano anatoka Kigoma kwa wakwe zangu kule unamleta Kinondoni hajui mahitaji ya Kinondoni na hafanyi consultations na urban authorities unatarajia nini.

Mheshimiwa Spika, na hii ndio unaikuta katika maeneo mengine kwamba kwa kuwa hakuna consultations na wao ndio wanaojenga barabara tunapata matatizo na matatizo hayo yanapeleka kwa mfano kule Kinondoni sisi si wakulima hatuna bahari hatuvui pale katika Jimbo la Kinondoni kazi yetu sisi ni biashara na uchuuzi na shughuli nyingine ndogondogo tunahitaji kutembea sana, tunahitaji barabara ambazo ziko nzuri ambazo zinapitika. Sasa ukiangalia pale kwetu utakuta tunahitaji moja kubwa la barabara ambayo ni kilomita tatu tu iko kuanzia pale Mtaa wa Mlandizi kule na inakuja inapita sehemu za makumbusho inakwenda kuhudumia, kata karibu nne.

Mheshimiwa Spika, sasa ningemuomba Mheshimiwa Waziri kwamba apate muda yeye ama wasaidizi wake twende nao Kinondoni wakaangalie pamoja na kwamba Kinondoni ndio Dar es Salaam, lakini hali ni mbaya sana za barabara na hasa mvua zinaponyesha tunakuwa na adha kubwa sana na ukiangalia Wananchi wa Kinondoni ni moja kati ya watu ambao wanachangia sana katika kodi za Serikali ikiwemo mapato ya pale Kinondoni kwenyewe ambako tunakusanya zaidi ya bilioni 40 kwa mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na hili ningeiomba Serikali sasa iweze ohh! my God! naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuchangia katika hotuba iliyoko mbele yetu. Kwanza napenda nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, yeye pamoja na wasaidizi wake kwa kazi nzuri. Hotuba yake hii imejaa matumaini mazuri sana kwa wananchi wetu wa Tanzania. Naamini kwa kuwa yumo ndani ya Serikali Sikivu, basi hata haya ambayo sisi Waheshimiwa Wabunge tunachangia, atayachukulia kwa uzito unaostahiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu nitaupeleka katika huduma za watoto yatima, nitazungumzia kidogo suala la maiti na nilikuwa nizungumzie Kampeni ya Nyumba ni Choo, lakini bahati nzuri Mheshimiwa Mbunge aliyepita ameshalizungumzia. Hata hivyo, kama nitapata nafasi, naweza nikaligusia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri na pia nimepata nafasi ya kuisoma tena. Kuna maeneo ambayo yananisikitisha kwamba hotuba hii haijataja kwa uwazi kabisa watoto yatima. Hili ni eneo ambalo, katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri ameligusia, watoto ambao wapo katika mazingira magumu, lakini nadhani ingekuwa busara tukawataja, kwa sababu nchi hii sasa hivi ina watoto yatima ambao wametokea tu katika lile kundi ambalo wazazi wao wamefariki kwa HIV, wako takribani 1,400,000 ukiachilia wale wengine ambao wazazi wamefariki wao katika magonjwa mengine na acts of God wameondoka, yawezekana kuna watoto wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hali hii, naomba sana Mheshimiwa Waziri afikirie. Yawezekana Taifa hili sasa linahitaji kuwa na sera specific kwa ajili ya watoto yatima. Kwa nini nasema haya? Nasema hivi kwa sababu najua kuna Sera ya Maendeleo ya Watoto ile ya mwaka 2008, lakini kutokana na hali halisi ambayo sisi Waheshimiwa Wabunge tunakumbana nayo katika Majimbo yetu, utaona ni hakika watoto yatima wanahitaji watu wa kuwasemea.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwishoni mwa wiki nilipata nafasi ya kutembelea vituo vinne vya kulelea watoto yatima katika Jimbo langu la Kinondoni. Nilikwenda katika Kata ya Hananasifu, nikaenda kwenye Kata ya Mzimuni, Kata ya Tandale na Ndugumbi. Niliyoyaona kule yawezekana kabisa yanaakisi hali ya watoto yatima katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa sababu hii napenda niwapongeze kwanza wale wananchi ambao wamejitoa, kwa sababu hawa ni wananchi wa kawaida na wengi wao ni akina mama ambao ni watu wazima, lakini wamejitoa kwa hali na mali. Wengine wana watoto 50, wengine wana watoto 200, wengine wana watoto 300, wanategemea wafadhili na wana kazi ngumu sana ya kuwapeleka shule watoto hawa, kuwafundisha tabia njema na utashangaa watoto wanajua dini, wana tabia njema pengine tofauti na hata watoto wetu ambao wako majumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia ni kwa jinsi gani Serikali inaweka mkono wake pale? Hili mtanisaidia Mheshimiwa Waziri, ni kwa jinsi gani Serikali inasaidia watoto yatima ambao wanalelewa katika mazingira ya kijamii. Labda niseme kitu kimoja, kuna hali ambayo badala ya wale watu wa ustawi wa jamii kusaidia na kuwapa moyo wale ambao wamejitolea, kuna wakati mwingine wanawakatisha tamaa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, nilifika katika kituo kimoja kinaitwa cha Bi Maunga pale Hananasifu; katika kukagua kagua nilikuwa namwuliza kuhusu upakaji wa rangi, maana kuna baadhi ya sehemu hazijapakwa rangi vizuri. Akasema suala hili pia liligusiwa na watu wa Ustawi wa Jamii, lakini badala ya kunisaidia, wamenitisha. Wanasema kama sikupaka rangi, watakifunga kile kituo. Kauli kama hizi siyo nzuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haya, mfano wakifunga kile kituo, wale watoto 100 wanakwenda wapi? Sasa lazima wafanyakazi wetu wa Ustawi wa Jamii wawe ni vijana au wawe ni akina mama au wawe ni watu wa rika lolote lile, wajifunze kuwa na customer care nzuri sana wanapozungumza na watu kama hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na changamoto nyingine na wengi wameizungumza, sasa sijui katika Majimbo mengine; watoto hawa wakipelekwa shule kuandikishwa, wanahitajika kuwa na Birth Certificate (zile hati za kuzaliwa) ambazo watoto wale ambao ni yatima waliopatikana katika mazingira ambayo mengine ni magumu, hawana hizo hati. Wanapata matatizo, hawapelekwi shule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali iangalie katika zile haki za Watoto, mojawapo ni haki ya kuendelezwa; haki ya elimu. Naiomba Serikali itoe kauli, naye atafute njia rahisi ya kuweza kusaidia watoto hawa kuweza kupata hati za kuzaliwa. Pale ambapo itakuwa na ugumu, angalau waanze kuruhusiwa kusoma huku taratibu nyingine zikitafutwa ili waweze sasa kupata elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine, wakati nazunguka nilikutana na wanafunzi kutoka Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, wanaosoma Saikolojia, walikuwa wanakwenda pale kuwapa nasaha wale watoto ambao wanajitambua. Jambo lile limenifurahisha sana. Kwa hali hiyo, naiomba Serikali itoe wito kwa vijana wanafunzi ambao wanasoma katika vyuo kama hivi wakipata nafasi watembelee maeneo ya yatima, wazungumze nao na kuwapa encouragement kwamba kuwa yatima siyo mwisho wa maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja la mwisho ambalo napenda nilizungumze kuhusu huduma za maiti. Huduma za maiti kule kwetu Kinondoni wakati tunafanya kampeni lilikuwa ni suala moja zito sana. Maneno ni kwamba, watu wanapofariki miili haitolewi mpaka watu walipie. Sawa, ni haki kabisa kulipia, lakini jambo kama hili linatakiwa Serikali ilitolee mwongozo ambao utasaidia kupunguza machungu ya watu wanaofiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweza kuruhusu watu wakapewa miili ile, yaani maiti wakaenda kuzika na kukawa na utaratibu mwingine wa kuweza kuzipata zile fedha, ama njia nyingine zozote ambazo zinawezekana. Ila lugha ambayo ilikuwa inatumika jamani, ni kwamba Serikali inatuuzia maiti. Maiti wanauzwa! Kwa maana huwezi kumpata maiti mpaka ulipe pesa. Nilikuwa naomba tu Serikali iweze kutafuta njia ambayo inaweza ikasaidia kuondoa machungu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili nami niweze kujadili taarifa ya Serikali za Mita. Mimi nitajikita huko.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kilio cha Waheshimiwa Wabunge wote, kila aliyesimama analizungumzia kwa uchungu mkubwa sana suala hili. Naomba tusimalize kwa kuzungumza peke yake, tuje na maazimio makali ili Bunge hili liwe ni mfano ambao mtu mwingine yeyote aweze kufanya reference kwamba Bunge hili chini ya Mheshimiwa Spika Dkt. Tulia walisimama wakakemea na wakachukua hatua kupinga ubadhirifu unaofanywa katika halmashauri zetu. Hiyo ndiyo opening statement yangu.

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye tathmini ya Mkaguzi. Ukifungua kwenye ukurasa wake wa tano, kwanza kabisa anasema, amefanya tathmini ya mifumo ya utawala ambayo tumeizungumzia na amebaini migongano ya kimajukumu kati ya wachaguliwa kwa maana ya Madiwani na watendaji. Hii migongano aliitolea mifano ya Wenyeviti wa Serikali za Mitaa au Madiwani kusaini Mikataba. Hapa ndipo penye matatizo na ulaji uko hapa. Ndiyo maana utakuta kwamba kwa kuwa tunafanya kazi pamoja, sioni Madiwani pamoja na sisi kuwa na political will ya kusimama na kukemea huu ubadhirifu. Kwa maana na sisi ni sehemu, si tunaitwa Madiwani na tunatoka katika halmashauri!

Mheshimiwa Spika, ukiangalia dhana nzima ya utawala bora inatuhitaji hata sasa katika Serikali za Mitaa tuwe na separation of powers. Hii dhana ambayo iko katika Serikali kuu inapaswa kushuka chini, madiwani tubakie au na kazi ya usimamizi na watendaji wafanye kazi za utendaji. Haya ndiyo matatizo, ingawa ndiyo sharti la kisheria la sasa hivi, lakini kwa miaka 38 mfumo huu haujatusaidia. Ni wakati wa kuungalia mfumo kwamba haufai.

Mheshimiwa Spika, kwa nini haufai? Hakuna ripoti ya CAG ambayo kwa mwaka mmoja itakuwa inaonesha kuna matumizi mazuri ya fedha za Serikali, hakuna. Kila mwaka kuna matatizo. Hebu chukulia mfano, fedha ambazo tunazipitisha hapa katika Bunge lako Tukufu, utakuta kati ya asilimia 60 mpaka 75 na kuendelea zinapelekwa katika Serikali za Mitaa, na kule ndipo tunapotegemea pajengwe shule, hospitali na huduma nyingine za wananchi wa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, ukaguzi huu haujaonesha pia pesa za COVID ambazo nazo zilikwenda kufanya kazi hiyo hiyo. Je, leo ukaguzi ungeonesha fedha za ndani zimeliwa hivi na fedha za COVID zimeliwa hivi, pangekalika humu ndani? Sasa nilikuwa nashauri kwamba kwa kuwa ukaguzi umefanyika, matokeo yametokea, ningemwomba CAG akaangalie pia fedha za COVID. Kwa sababu ukiisoma hii taarifa kuna mambo mengi sana hasa yale ya re-allocation yaliyofanyika.

Mheshimiwa Spika, fedha imeingia, inaonekana hii imekwenda kujenga shule fulani; na hii imetokea pale kwenye jimbo langu. Shilingi milioni 600 zimeletwa kwa ajili ya Secondary School Tandale, zimeondolewa zikapelekwa mahali pengine na shule haijajengwa. Haya mambo hayakubaliki. Ukiangalia haya yote ni kwamba hawa watu hawana uwoga kabisa. Wamejawa na dharau na siyo dharau tu, na jeuri, naweza kuthubutu kusema ni jeuri kwa Rais na kwa Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unawezaje kupewa maagizo na Kamati ya LAAC, Kamati ambayo ni sehemu ya Bunge; kamati ikizungumza Bunge limezungumza. Kamati inatoa maagizo, wewe huyatekelezi, kama siyo dharau maana yake ni nini? Kuna tafsiri nyingine yoyote hapo? Bunge linaelekeza ukafanye moja, mbili, tatu, nne, nawe huyafanyi, unatarajia nini? Unatarajia kwamba huna utakachofanywa. Ndiyo maana kwenye opening statement yangu nimesema na kila mtu amezungumza, kwamba lazima tuje na mfano kwamba hawa watu, hatua za kishera zianze kuchukuliwa. Kama ukaguzi huu ni sampling bases ten percent: Je, hizo asilimia 90 zingeonesha nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mengine humu yanaonesha kabisa ni uhujumu Uchumi. Unapokeaje risiti ya kugushi. Jamani Waheshimiwa Wabunge, risiti ya kugushi inatafsiri ngapi? Inatafsiri kwanza kuna makosa ya kugushi; pia kuna tafsiri ya uhujumu uchumi ndani yake. Tumewaona hapa miaka miwili, mitatu iliyopita watu wanaotiwa ndani kwa ajili ya uhujumu uchumi. Lina tafsiri gani hili suala kama siyo uhujumu uchumi? Ukiikosesha mapato Serikali na ukiyatumia mapato ya Serikali visivyokusudiwa, yote hayo ni makosa. Tukikaa kimya na hili likapita; na humu ndani naona CAG ametumia lugha nyepesi, anawaambia TAMISEMI chukueni hatua hizi; maeneo machache, TAKUKURU chukueni hatua hizi.

Mheshimiwa Spika, Bunge lako liazimie kwamba wale wote wenye dalili za kijinai katika ripoti hii watambulike walipo na wachukuliwe hatua. Kila ambaye amefanya kosa la dalili za kijinai za ubadhirifu wa fedha za Serikali achukuliwe hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sisi Wabunge hapa tumedharaulika sana wakati tunapitisha tozo, wametusema sana katika mitandao ya kijami. Uongo, kweli! Tumesemwa sana! Zile fedha tukazipata, tukazipeleka huko kwenye kujenga shule, barabara na ndiyo fedha hizi ambazo zimeliwa au hazionekani. Kama hatukuchukua hatua, leo wananchi watatuona ni watu wa namna gani?

Mheshimiwa Spika, kuna fedha nyingine zinapelekwa katika uwekezaji wa mitaji ambayo haina faida. CAG anazungumza na ametoa mifano kwamba Halmashauri sasa zinaigana katika kutengeneza miradi ya kuwekeza na wengine walikwenda kuwekeza hata katika mabenki. Kuna benki moja waliwekeza karibu share 24,000 ambazo zina thamani ya Shilingi bilioni nne. Sasa hivi shares zile zimepungua zimekuwa za Shilingi bilioni moja. Hakuna faida kwa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, kama kuna sheria ambayo inasimamia mamlaka za Serikali za Mitaa kwenda kuwekeza, tuilete hapa Bungeni tuifanyie marekebisho. Yawezekana kuna mambo mengine yanafanyika hatuyajui na hii ni sehemu ya asilimia kumi ya ukaguzi. Je, tungekwenda kwenye kila Halmashauri kuona wanawekeza wapi; wanafanya nini? Ni dhahiri kabisa tutakuta kuna fedha nyingi zimepotea.

Mheshimiwa Spika, kuna dharau nyingine. Mkaguzi anakuja anagundua kuna hoja 10,824; zimetekelezwa 3,511 tu ambayo ni asilimia 32. Asilimia 35 hazikuguswa kabisa. Hii ndiyo ninayosema kama siyo dharau ni nini? Wanajua kama hukutekeleza mwaka wa kwanza, wa pili, wa tatu, kama vile tutakavyobadilisha Bunge, Wabunge wakiondoka wanaopiga kelele kama akina Tarimba hawatakuwepo, yatapita. Haya ndiyo mazoea ambayo tumeyajenga. Bunge hili lisikubali. Kwa hali hiyo, tufanyeje?

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza nilikuwa nashauri, mfumo mzima wa Serikali ya Mitaa Sheria ile sasa imechoka, inahitaji kuangaliwa. Sheria lazima tuifumue, hata Rais mwenyewe amesema, ameona udhaifu alipokuwa amepokea hii ripoti, akawataka TAMISEMI waangalie. Tuangalie mifumo iliyopo haitusaidii, itupeleke kwenye separation of powers ikiwezekana, kila mtu afanye lake, usimamizi uwepo.

Mheshimiwa Spika, sisi Waheshimiwa Wabunge sioni sababu ya kuwemo katika Halmashauri. Kama hali yenyewe ndiyo hii, maana yake na sisi tunajumuishwa. Wewe sio Mbunge; Mbunge ni Mbunge na Mbunge ni Diwani, leo tutakataa vipi ule uozo ambao umefanyika kule kama sisi sio sehemu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye kamati za fedha sisi ni Wajumbe, ndiyo yanayofanyika humo. Wanafanya vikao sisi hatupo, na muda mwingi sana tuko Dodoma, halmashauri zinakutana katika mabaraza sisi hatupo. Tunaandikwa pale hakuhudhuria kwa taarifa, lakini maana yake ni sehemu ya maamuzi yanayofanyika. Sasa maamuzi yale kama yanatisha kiasi hiki na sisi tumo mle ndani, naomba kati ya mambo ambayo tuangalie, ni Wabunge tusiwe Madiwani ili tuweze kuisimamia na kuishauri vizuri Serikali, Serikali Kuu na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niwe mchangiaji wa kwanza kabisa katika hotuba aliyoitoa ndugu yangu Mheshimiwa Bashungwa.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nataka niseme kwamba naunga mkono asilimia mia moja hotuba hii na ninataka nimpongeze kwa kazi nzuri, hotuba nzuri yeye mwenyewe binafsi pamoja na wasaidizi wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka nichangie katika maeneo mawili makubwa; eneo la kwanza, ni uendeshaji wa mpira wa miguu katika nchi hii na eneo la pili, nataka nizungumzie kuhusu timu yetu ya Taifa ya mpira wa miguu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na mazungumzo haya naanzisha kutoka kwenye page namba 46 ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri pale ambapo amevitaka vyama vya michezo nchini kuendeshwa kwa mujibu wa taratibu za utawala bora, kufuata kanuni zao na vilevile kuhakikisha kwamba michezo inaleta tija na kuleta maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kutokana na hili nilitaka nizungumze kwanza upande wa mpira wa miguu. Mpira wa miguu ndiyo mchezo unaopendwa sana katika Tanzania, ipo michezo mingine, lakini mpira wa miguu ndio unaoshika namba moja na kutokana na hali hiyo mpira wa miguu umekuwa ni ajira, umekuwa ni biashara, lakini vilevile imekuwa ni maeneo ambapo watu wanapata burudani na kuwaliwaza wale ambao wanapata matatizo ya aina fulani na kwa fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwa bahati mbaya sana uendeshaji wa michezo hii umekuwa mara nyingi sana kumekuwa na changamoto za ajabu, mara nyingi uendeshaji hauridhishi, wadau wanalalamika na utakuta mambo mengine ambayo yanatufanya tulalamike wala hayana sababu ya kulalamika. Kwa mfano unakwendaje kubadilisha ya mchezo mzito kabisa, mchezo ambao watu wamewekeza kwa hali na mali kwenye furaha zao, wengine wametoka mbali sana wametoka Dodoma kuja kule Dar es Salaam, unakwenda kutubalidilishia mchezo mwisho mwisho wa siku. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naambiwa kuna watu walichungulia katika darubini zao wakaona wanakwenda kupigwa mabao basi wakaenda kufanya mipango ya kuweza kuupeleka mbele mpira ule, sasa tarehe mpya inakuja tuone watasogeza tena? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, viongozi wa klabu wamekuwa wakipewa adhabu za.., nitatumia neno ambalo siyo zuri, za hovyo hovyo kabisa, hakuna standard, leo huyu akifanya makosa yaleyale anapona mwingine akifanya makosa yaleyale anaadhibiwa kesho yake na adhabu za kutisha kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda mbali zaidi unakuta hata waamuzi wameathirika nao, wamejiingiza katika mambo kama hayo, wanafanya mambo ya upendeleo wa dhahiri uwanjani, wanakosesha klabu nyingine ushindi kwa sababu tu ya mapenzi yao wakijua kwamba watafungiwa mechi moja au mbili halafu wanarudi tena uwanjani. Mambo kama haya yanaleta taabu na kwa hali hiyo utakuta malalamiko yanapelekwa TFF leo, kesho yanapatiwa majibu, mengine yanakaa miezi miwili mpaka miezi saba, standard ipo wapi na hapa napata mashaka kwamba ndani ya chama chetu kile au federation hakuna uadilifu hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na yanapeleka mpaka mwisho yanafikia very personal, mnakutana katika sherehe, kwa mfano kama juzi kulikuwa na sherehe ya first division, watu wanapeana mikono, sijui ni jana, sijui watu wanapeana mikono wengine wanakataa kutoa mikono, wanatuonesha nini? Kwa sababu tu ya mapenzi yao. Mpira wa miguu umekuwa tented vibaya sana Mheshimiwa Waziri. Tusafishieni mpira wa miguu katika nchi hii ili uweze kutuletea matumaini yanayotarajiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na haya mambo yanayofanyika sasa hivi yanaathiri vilevile timu yetu ya Taifa, timu ya Taifa ya Tanzania haina matumaini, haina matumaini kabisa utafikiri timu ya Uingereza bwana! Uingereza ndiyo nchi za kwanza duniani ambazo zimewahi kucheza international competition. Mwaka 1872 wakicheza na Scottland wakatoka zero-zero, hebu fikiri timu kama hiyo imeshiriki na kupata ubingwa wa World Cup mara moja katika miaka yake yote, walipata mwaka 1966, lakini wana timu nzuri sana, timu zao za binafsi zile moja moja kina Chelsea, kina Manchester United na City wanacheza mpira mzuri sana kwa sababu gani, wao wameamua ku-commercialize ligi yao.

Mheshimiwa Spika, ligi yao ni nzuri sana katika dunia, wachezaji wote wazuri wanakimbilia kule. Lakini timu yao ya Taifa haioneshi ule ukali wa ligi yao, so it is the opposite, inavyotakiwa ligi ya nchini kwako hasa premier league ndio iakisi timu yako ya Taifa. Sisi timu zetu ziko kali, zina ligi, ligi yake inaanza kuendelea kuwa vizuri zaidi, lakini where is local talent, iko wapi local talent? Tunaletewa wachezaji wengi wa nje, timu zetu zinafanikiwa, lakini zinafanikiwa kwa sababu ya wachezaji sana wa timu za nje ambao pia nao ni wa mashaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa nini wa mashaka, wewe ukiangalia naomba niitaje baadhi ya timu, ukiangalia pale kwetu Young African kwa mfano, tunao wachezaji wa nje wengi tu, lakini hawaisaidii Young Africans mpaka iingie kina Kaseke na kina nani ndio watuletee magoli. Simba Sports Club wachezaji lukuki wamo mle ndani sijui, wachezaji saba mpaka nane kwa timu moja wanaocheza uwanjani, akiingia Boko ndio analeta maneno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa point yangu ni nini, point yangu ni kwamba ili tuweze kupiga hatua ningependa intervention ya Serikali kwa maagizo kwa TFF kwamba bwana sasa ni wakati wa kuangalia suala zima la wachezaji wa nje na jinsi gani ligi zetu zinaweza zikaibua local talents na timu yetu ya Taifa iweze ikasimama. Bila wachezaji wa ndani kupata nafasi za kutosha, wakacheza katika timu zao, tusahau kupata mafanikio katika timu ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpira wa miguu kama nilivyosema ni mchezo ambao unaotegemewa sana. Sasa kama utakuwa na premier league ambayo haiakisi mafanikio ya timu ya Taifa tutaendelea kubakia kama England. Sisi tumeshiriki mashindano ya ubingwa wa nchi huru za Afrika nafikiri mara mbili, Nigeria na juzi hapa Misri, lakini kote huko hatujapiga hatua, kwa sababu gani; hata uchaguzi wetu wa makocha, kocha akija hapa akikaa miezi sita ameshatimuliwa tayari, continuity unaipata wapi Mheshimiwa Waziri? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, watu wanatakiwa kustahamili na hiyo imeathiri mpaka kwenye klabu zetu sisi za mjini humo. Young Africans sijui katika msimu huu wameondoa makocha wangapi! Hata makocha wazuri huwezi ukamjua kama huyu mzuri kwa sababu ndani ya miezi mitatu hata hajapoteza mechi nakumbuka ameondolewa. Ukija Simba Sports Club nako ni hivyo hivyo, ukienda kwenye klabu nyingine ndogo ndogo ni hivyo hivyo. Hebu watanzania tuwe na tabia ya kustahamili tunapowapa makocha timu zetu kutulelea na hili nalitaka sana kwenye upande wa timu ya Taifa Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwamba timu ya Taifa muisaidie na katika kuisaidia sio kuwapa fedha tu, wapeni maelekezo yanayofaa na najua Serikali haitakiwi iingilie masuala ya mpira, lakini jina la Tanzania ndilo linalotumika. Tukifanya vibaya nchi yetu kama nchi ndio inayopata ratings mbovu, tusikubali Tanzania ipate ratings mbovu kwasababu ya viongozi ambao hawajitambui. Hawa viongozi wasiojitambua wanaopewa mamlaka ya kuongoza TFF, Mheshimiwa Waziri wawekeeni taratibu ngumu sana ili hata kupima uadilifu kwa timu zetu za Taifa, kupima uadilifu wao kwa Tanzania uwe ni moja ya vigezo vya kupata viongozi wa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sio tu kura, msiangalie sana suala la kura, kama mtu tunamuona akienda kwenye kupigiwa kura atashinda, muondoeni. Mbona wangapi wamekatwa katwa katika nafasi chungu mzima, kwani kuna lazima wawe ni wao wao tu? (Makofi)

Mheshimiwa Waziri naomba nikuunge mkono katika mipango yako ambayo umeizungumza ya mwisho. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuchangia.

Mheshimiwa Spika, vilevile nimpongeze mwananchi mwenzangu, Mheshimiwa Mwigulu, kwa hotuba nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ninapenda nitumie aya moja katika Surah Al-Fatiha iniongoze kwa haya ambayo nataka niyaseme. Aya hii inasema iyya qa budu-wa iyya qa nastaeen. Tunamwambia Mwenyezi Mungu kwamba wewe ndiye tunayekuabudu na wewe ndio tunayekuomba msaada.

Mheshimiwa Spika, msaada ninaouomba leo hii kwa Mwenyezi Mungu ni kwamba amuongezee busara nyingi sana mwananchi Mwigulu Nchemba, haya maneno yaliyotolewa na Wabunge basi uyapokee. Na ikiwezekana vilevile kwa kuwa umefanya vizuri sana katika hotuba hii, utupatie pia mchongo tarehe 03, Julai mambo yanakwenda kuwa namna gani, itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nianze kwa kupongeza hatua kadhaa ambazo Serikali ya Awamu ya Tano imechukua katika masuala mazima ya ukusanyaji wa mapato pamoja na Serikali ya Awamu ya Sita, lakini inatiwa doa na watu wachache pale Ministry of Finance. Watu ambao wameamua kwenda kujichotea mapesa kama vile Sakata la Mheshimiwa Waziri Mkuu lilivyoeleza.

Mheshimiwa Spika, naiomba Serikali; fanyeni history. Fukuza kila mtu aliyemo katika mnyororo ule, hata kama ni mkubwa kiasi gani. Kwa sababu tumechoka, sisi tunaomba barabara, tunaomba dispensaries, Waziri anasema fedha zikipatikana. Fedha zinapatikana watu wamechukua. Halafu unasema kwamba fedha zikipatikana. Zipatikane mara ngapi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Gavana wa Benki Kuu. Juzi tulimuuliza katika Kamati; wlae waliosababisha bureau de change zitumike vibaya na kuiletea Serikali hasara, hawa watu bado wako kazini? Akasema amewafukuza watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ameweza kufanya Gavana, Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, unawasubirisha nini hii mijitu hii? Inatuletea tabu. Na ndiyo maana kuna baadhi ya votes (mafungu) wanaweka fedha zao mle, wanazificha mule ili wapeane maposho a vile hakuna Serikakamli. Hili suala naomba mliangalie.

Mheshimiwa Spika, na namuomba sana Mheshimiwa Mwigulu, mchango wa Kamati, hotuba ya Kamati ya Bajeti ambayo ni mjumbe, naomba aiangalie sana. Mle ndani mna madini kwelikweli; kayafanyie kazi na hakika ataboresha vizuri zaidi utaratibu wa uendeshaji wa Wizara yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninapenda nipumue kitu kimoja new thinking katika mawazo ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge. Namba moja, nafikiri kuna kitu unakifahamu Mheshimiwa Saashisha hapa aliwahi kuwaona Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Kamishna Mkuu wa TRA, kuna kitu ambacho kimebuniwa na Watanzania, vijana hawa wa IT, kinaitwa Simply Tech kinachokwenda kujaribu kuongeza mapato katika ukusanyaji wa mapato, utoaji wa risiti, utengenezaji wa mahesabu ya mfanyabiashara lakini vilevile kwa faida ya TRA.

Mheshimiwa Spika, naomba sana hao Watanzania ambao wanakuja na kubuni mambo ambayo yanaweza yakaleta masuluhisho katika matatizo ya utoaji na upokeaji wa risiti, hebu Serikali liangalieni hili ili muweze kuona kwamba hawa vijana wetu wanachangia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la TRA; TRA tumekubaliana kwamba private sector ndiyo engine ya uchumi wa nchi hii. Na tukaenda mbali, hata katika michango ya Waheshimiwa Wabunge, kuonesha ni jinsi gani matatizo ya ulipaji kodi yapo.

Mheshimiwa Spika, nataka niangalie upande mmoja, kwamba wafanyabiashara wanalalamika kuhusu ucheleweshaji wa kufanyiwa tax audit. Niliwahi kulizungumza hapa. Lakini tukafikiria kwamba ni jambo jepesi, kwamba mfanyabiashara hafanyiwi tax audit hadi miaka miwili au mitatu iwe imeshapita; inatengeneza interest, inatengeneza penalties. Kiasi kwamba hata mwisho wa siku inapoletwa hesabu yake hata fedha za kulipa hana kwa sababu anakula mtaji wote.

Mheshimiwa Spika, katika utafiti mdogo niliofanya nilitembelea Mkoa wa Kikodi wa Kinondoni nikazungumza na viongozi pale. Tatizo jamani siyo TRA, tatizo ni Serikali hawataki kuwapatia wafanyakazi wa TRA idadi kamili ya wafanyakazi wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, niwape habari; Mkoa kama wa Kinondoni ambao unapokea kitu wanachoita tax returns zaidi ya 10,000, lakini ina tax auditors 24, kila tax auditor mmoja, au wote hawa kwenye tax plan watengeneze na kujibu tax cases 360; ni lini watafikia returns 10,000?

Mheshimiwa Spika, na ndiyo maana hata hizi fedha ambazo zinawekwa malengo ya kukusanya naziona ndogo sana. Mkiwapatia wafanyakazi wa kutosha TRA nina hakika wataweza kufanya vizuri. Kinondoni pamoja na uchache wa wafanyakazi wamepangiwa mwaka huu wakusanye bilioni 820, ninavyozungumza wameshafikia asilimia 92; kwa uchache wao. Suppose mnawapatia wafanyakazi wa kutosha?

Mheshimiwa Spika, kule kuna vitu wanaita blocks management ambapo wao wanahusika na masuala yote ya tax compliance. Kila block moja ina watu wanne mpaka watano, hebu niambie Mwananyamala kuna watu wangapi pale ambao wanafanya shughuli za kibiashara, wanafikiwaje na watu hawa wanne/watano huo ni mzaha!

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana kila Mbunge akisimama anaiomba Serikali, Mheshimiwa Mwigulu naomba unisikilize, tuongezeeni wafanyakazi TRA kwa sababu tunahitaji kukusanya fedha zaidi. Idadi ambayo mmeitangaza juzi tarehe 1 Juni, eti mnakwenda kuajiri watu 48, siyo mzaha huu? Ndiyo maana shemeji yangu Kilumbe anauliza ni busara? Hivi kweli ni busara watu wanahitaji wafanyakazi mkaajiri watu 48 mnawapeleka wapi, Kinondoni au Ilala maana huko ndiyo kwenye fedha nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa hebu fanyeni kitu kimoja, Rais aliyepita Mheshimiwa Jakaya anasema huwezi kula bila kuliwa, hebu tuajiri watu tuwalipe mishahara watufanyie kazi. Tusing’ang’anie watu wachache tuwape malengo madogo wanayatimiza tunawapigia makofi, kuna fedha nyingi huko nje, returns 10,000 plus halafu kwa mwaka unashughulikia kesi 360 yawezekana vipi? Ndiyo maana watu wanapiga kelele kwamba mnawacheleweshea kuwakagua kwa sababu hakuna wafanyakazi wa kutosha.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine tunazungumzia EFD machines, tena huko ndiyo kwenye matatizo. Kinondoni Region ina watu wanne halafu tunasema masuala ya kudai risiti na kutoa risiti, watu wanne kwenye mkoa mkubwa kama ule Tanzania, hakuna mkoa mkubwa Tanzania zaidi ya Kinondoni. Ni busara kweli Mheshimiwa Mwananchi mwenzangu, watu wanne EFD machines halafu huku tunasema watu hawadai risiti na hawatoi risiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nazungumza haya lakini ni mambo ambayo yanafanya hata ukusanyaji wa kodi uwe ni wa mashaka. Nina hakika kabisa Serikali sikivu kama ya Mama Samia Suluhu Hassan na Mwananchi pale pamoja na Waziri Mkuu mkienda mkikaa mkifanya caucus yenu angalieni suala la kuongeza idadi ya wafanyakazi ndani ya TRA you will never go wrong. Hiyo mtakuja kutuambia kwamba Wabunge kweli mmeiwashauri Serikali vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba nimalize kwa kusema nampongeza Mwananchi na vilevile naiunga mkono hoja iliyopo mbele yetu. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante nakushukuru sana na mimi nipate nafasi ya kuchangia katika Mapendekezo haya ya mpango ambayo yameletwa na mwananchi Mheshimiwa Mwigulu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nipende kuunga mkono hatua iliyofikiwa hadi sasa naunga mkono mapendekezo haya. Vilevile niipongeze Kamati ya Bajeti tulifanya kazi nzuri sana ambayo hata Waheshimiwa Wabunge humu wameikubali na kwa hali hiyo ningeomba Mheshimiwa Waziri ayachukulie kwa uzito stahiki kabisa mapendekezo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitazungumzia katika vile vipaumbele na ningeanza na maendeleo ya watu. Kwenye Jimbo langu la Kinondoni sisi hatulimi, hatuna bahari hatuvui, sisi ni watu wenye shughuli ndogo ndogo na tunawamachinga wengi sana na mimi sitaki nizungumzie eneo la wamachinga kama lilivyozungumziwa ile timua timua, upangaji, hapana mimi nakubaliana na Serikali hatua walizochukua. Nataka niliangalie eneo hili hasa pale ninapolinganisha na mpango kwamba mpango wenyewe huu haujabainisha hali ya umaskini kiwazi kabisa na jinsi gani mpango unakwenda kuhangaika na taratibu za kuondoa umaskini, hii inaunganisha na wamachinga kwa sababu hili kundi limejitokeza miongoni mwetu na ni kundi ambalo yawezekana kabisa na naamini Serikali haijawahi kufanya utafiti kulijua kundi la wamachinga lina nguvu kiasi gani katika uchumi wa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yawezekana tunawaona tu barabarani wakitembea ama wakijenga mabanda yale ya plastiki, lakini nataka nikwambie kwamba hawa watu kwanza wamewaondolea mzigo Serikali ya kuwatafutia kazi ni watu ambao wameamua kujiajiri wao wenyewe, lakini kama itafanyika tafiti ili kuonekana kwamba hawa wamachinga ni kwa jinsi gani wana-support baadhi ya viwanda vidogo vidogo nchini, baadhi ya wakulima wanaouza matikiti utakuta kwamba sasa hivi biashara imeshuka kidogo kwa sababu hawajakaa vizuri zaidi maana yake nini maana yake wanamkono katika uchumi, wana mkono katika biashara katika Taifa letu kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri mpango huu ujaribu kuunda utaratibu wa kwenda kufanya utafiti wa kina very independent ili kuliangalia hili kundi hili la wamachinga ni kundi la aina gani lina nguvu kiasi gani katika uchumi ili kama ikiwezekana waliingize katika utaratibu wa kulipia hata kodi wajulikane wanafanya shughuli gani na wapo wapi na akina nani ili nao waweze kuchangia katika Pato la Taifa la nchi yetu, lakini vilevile katika kodi za Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba nizungumzie ukurasa 25 na 26 za Mheshimiwa Waziri wakati alivyokuwa akitoa hotuba yake juu ya kuwasilisha kwa mapendekezo haya na hii inagusa vipaumbele vifuatavyo: -

Kuchochea uchumi shindani, kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani, utoaji huduma na kukuza biashara na uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote haya ukiyaangalia yanagusa mwenendo wa kibiashara na hasa private sector na kwa kuwa private sector ni tegemeo kubwa sana katika kodi za Taifa hili kiasi kwamba zaidi ya trilioni 22 zinatarajiwa kutoka kwao. Kwa hali hii nilikuwa naangalia ni kwa jinsi gani basi hivi vipaumbele vitatu vinaweza vikaleta mafanikio bila ya kuangalia ni kwa jinsi gani private sector inakwenda kusaidiwa. Hebu tuangalie nijaribu kukumbusha huko nyuma kulikuwa na kitu kinaitwa road map for improvement of business and investment climate baadaye ikaja big results now sasa tuna blue print.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zote hizi ni documents ambazo zilikuwa zinajaribu kutatua na kuleta hali bora ya uendeshaji wa biashara katika Taifa hili. Nimeangalia katika huu mpango sijaona vizuri ni kwa kiasi gani blue print imefyonzwa katika Mpango huu sijaiona yaani ikaja wazi wazi kabisa, kwa sababu blue print yenyewe ni majibu ya matatizo tuliyonayo katika kuifanya private sector ikawa vibrant na ikaendelea kuchangia kiasi kikubwa, trilioni 22, kwa Tanzania ya leo ilivyo ni fedha ndogo mimi ninaamini kabisa, laiti kama tungeshika certain buttons tukaminya vitufe ambayo pengine hatuvijui au tunavijua kupitia kwenye blue print utakuta kwamba uchumi wa Tanzania utafunguka hasa katika kipindi sasa Tanzania tumejenga imani huko nje, tumejenga imani ndani, kwamba sasa Tanzania unaweza ukafanya biashara vizuri. Ingawa Tanzania kufanya biashara ni kugumu kidogo kwa sababu hata kwenye index ile ya easier of doing business bado hatujafanya vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba mpango huu uje na hatua za kutunasua kule kufanya vibaya katika ufanyaji wa biashara tuondoke katika ile nafasi ya 141, tupande juu ili tuweze kuwavutia watu wengi sana. Kutokana ninaomba mpango uje kiwaziwazi uonyeshe ni kwa jinsi gani tutakwenda kuondoa urasimu wa ufanyaji na mifumo ya usimamizi wa biashara katika nchi yetu, regulator reforms lazima zifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine tusaidie Mpango uweze kuja wazi wazi utuondolee gharama nzito za kufanya biashara, leo hii ukifanya biashara regulators walio wengi watakufuata, wewe ukisoma ile sheria ya OSHA peke yake kuna kodi ya kucheka, kuna kodi ya kuchukia yaani ni hatari ni hatari kabisa, ukitoka hapo ukienda kwenye fire nao wana mambo yao yaani ni balaa balaa, hebu tufanye ufanyaji wa biashara katika nchi hii usiwe na gharama kubwa ili tuweze kuwavutia watu wetu wengi wafanye biashara, Watanzania na hata wale wa nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala hili la reduction...

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Waziri wa Nchi.

T A A R I F A

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamheshimu sana Kaka yangu Tarimba Mheshimiwa Mbunge, lakini naomba tu tuwe realistic katika sheria zote ambazo zimetungwa na sheria hii, hamna tozo yoyote iliyowekwa na Serikali ambayo inamtoza mtu kwa kucheka, inamtoza mtu kwa kukasirika ama kuchukia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani tukiacha hivi records zetu zitakuwa zimerekodi kitu ambacho hakina uhalisia kwa hiyo nilikuwa naomba nimpe taarifa kodi hizo ndani ya Serikali hatuna. (Makofi/Kicheko)

MWENYEKITI: Unajua Yanga hawa wana shida sana, Mheshimiwa Tarimba unapokea taarifa. (Kicheko)

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naipokea. Unajua alikuwa Makamu Mwenyekiti wa Baraza la Michezo, tulikuwa pamoja sina haja ya kushinda naye ni kweli hakuna kodi hiyo lakini inaonesha vile vikodi vidogo vidogo vya kuangalia ngoja kuna kodi ya vision sijui kufanya nini wanakupima macho, kama kampuni kama mtu, kuna vikodi vingi vingi hata Mheshimiwa akitaka nimkumbushe, nimuoneshe, nitamuonesha, lakini zipo kodi zinazoudhi ninachojaribu kusema ni kodi zinavyoudhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ningependa nione huu mpango unakuja na ile dhana ya kuongeza confidence kwa investors wa ndani na wa nje, watu waliumiaumia hapa katikati hivyo, ningeomba mpango huu uweze ukasaidia.

Kwa hali hiyo, kwa kuwa nimeyazungumza yale ambayo nilikuwa nataka kuzungumza niseme naunga mkono hoja hii. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kuchangia kuhusu taarifa za kamati ambazo zimewasilishwa leo. Kwanza kabisa naomba nianze kwa kusema naunga mkono hoja hizi lakini nianze vile vile kwa kumtaja Mwenyezi Mungu na niruhusu niseme Bismillah Rahman Rahim. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumzia maji kama ilivyokwenye ukurasa 27 nikipata muda nitazungumzia page 12 taarifa ya Kamati ya Bajeti. Mimi ni mjumbe wa Kamati ya bajeti na kwa hali hii nazungumza mambo ambayo nayafahamu vizuri zaidi. Juzi tulikuwa na mazungumzo na Mheshimiwa Waziri wa Maji na katika Mazungumzo yale tulizungumzia masuala ya RUWASA, tukaona ugumu wa matatizo ya maji ambayo yako vijiji, tutakaa miaka mingi sana bila ya matatizo ya maji kuweza kupatiwa ufumbuzi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, na Tanzania hii na Bunge hili hakuna siku ambayo inapita bila Mbunge yoyote kusimama kuzungumzia habari ya maji maswali ya maji yamekuwa ni mengi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali na kwenye hili tuige mfano mzuri wa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan alipokwenda kutuletea fedha za mkopo ambazo zimeondoa matatizo ya shule za Sekondari katika Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimemwambia Mheshimiwa Waziri wa Maji kwamba hebu nendeni kwenye kila Wilaya angalieni mahitaji ya maji, angalieni vyanzo vya maji viko wapi tengenezeni mpango ambao utaiangalia Tanzania nzima ni wapi kwenye matatizo ya maji ni wapi maji yanapatikana hata kama ni kumshauri Mheshimiwa Rais akope fedha tumalize masuala ya maji, Bunge hili linaweza likaweka alama kubwa sana Bunge la Kumi na Mbili kwamba angalau asilimia 80, 90 ya matatizo ya maji yanaweza kwenda kumalizwa, tukope, kuna hasara gani ya kwenda kukopa kwa ajili ya mtanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba iingie katika Kumbukumbu na Mheshimiwa Waziri wa Maji sijui kama yuko hapa, lakini hachukue hilo kwamba Bunge hili kwamba limechoka kusikiliza maswali ya maji kila siku wakati tunaweza kupanga tukayaondoa matatizo ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jingine kuna kitu ambacho nashangaa sana mwaka 2015 na hili linahusiana na page 12 ambayo inahusiana na hushirikishwaji hafifu wa sekta binafsi. Serikali haifanyi biashara, Serikali kazi yake kuweka mazingira mazuri ya kufanya biashara ili iweze ika-collect Government Revenue fedha kutokana na kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2015/2016 walitengeneza kitu kinaitwa Blue Print na wakakitoa mwaka 2018 mwezi mei na ikaeleza vizuri sana ni jinsi gani inavyokwenda kuboresha maslahi ya ufanyaji biashara kwa madhumuni ya kupata fedha ya kutosha katika Government Revenue. Na wakati ule easy way of doing business, watanzania sisi tulikuwa ni nchi ya 131 mwaka 2015 wakati ikitolewa hii ripoti tulikuwa sisi ya watu 141 katika nchi 190. Maana yake ni nini? Tulikuwa bora kabla ya Blue Print haijatengeneza Blue Print imetengenezwa ndiyo tumeanguka na tatizo lake kamati inasema mpaka leo hii wingi ya mamlaka za udhibiti zinaendelea kuongezewa kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia tozo zimejaa, ukiangalia ada kwenye biashara moja zimejaa, ukiangalia huku matatizo ya kodi siyo rafiki, mimi najiuliza ni kwanini basi tulitumia fedha kutengeneza Blue Print halafu ni sawa saw ana mtu uchonge kinyago halafu kile kinyango ukikiangalia unakiogopa eeh, tunatengeneza Blue Print tumeweka kwenye kabati hatuitumii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ituletee taarifa kamili ya jinsi ilivyotekeleza Blue Print katika kipindi chote hicho ili tuweze kufanya tathimini na kujiuliza ni kwanini hatutoki katika idadi ile ya 142.

NAIBU SPIKA: Ahsante!

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana nakushukuru message sent. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, nimepewa salamu na wananchi wa Kinondoni nimletee Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba wao wanafurahishwa sana na utendaji wako wa kazi. Wanakuona kila mahali kwenye migogoro kwenye utatuzi wakasema huyu Waziri Mkuu tulienaye anafanana sana kama ile timu iliyotengeneza gap ya point 10 haishikiki! Mimi naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu uendelee na kasi hiyo hakuna mtu atakayekugusa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii nimpongeze Mheshimiwa Rais, alipokuja pale Kinondoni kwa ajili ya kuzindua yale majengo ya Magomeni Quaters ambapo wananchi 642 wamepata makazi mapya, hakika wananchi wa Kinondoni wamefurahia sana na sikuwa nimepata nafasi ya kuzungumza, lakini nataka nimwambie kupitia Bunge lako Tukufu, Mheshimiwa Rais wananchi wa Kinondoni wamefurahi sana na wanamuombea kila la kheri, Mwenyezi Mungu amjalie afya njema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanasema haya kutokana na jinsi Serikali inavyofanya kazi yake kwenye eneo hili la Kinondoni, tunasubiri mradi ambao utaanza mwezi wa Julai inshallaah ambao ni mradi wa Mto Msimbazi, maeneo ambayo yalikuwa yanapata mafuriko kila wakati, maeneo ya Kigogo, maeneo ya Mzimuni, maeneo ya Magomeni, yanakwenda kupata sura mpya kwa mradi wa Shilingi Bilioni 240 na zaidi.

Mheshimiwa Spika, wananchi wale wanachokiomba Mheshimiwa Waziri Mkuu naomba hili uli-note, kwamba zitakapokuja taratibu za kulipa fidia basi zifanywe kwa wakati. Kwa sababu wana hofu na lile lililotokea katika Kata ya Magomeni, Mtaa wa Suna, Kata ya Hananasifu, Mtaa wa Kawawa na Mtaa wa Hananasifu yenyewe na Mkunguni, wananchi wamevunjiwa njia nyumba zao Mheshimiwa Waziri Mkuu katika kipindi cha mwaka 2015/2016, Wizara ya Afya pamoja na watu wa mazingira walikwenda kuvunja zinazofikia 945 wananchi wale mpaka leo wanapata shida, hakuna wakuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, sitaki niyazungumze haya mengi nitaomba Mheshimiwa Waziri Mkuu unipe nafasi nikutane na wewe ili nilete hiki kilio cha wananchi wa maeneo kwako na uone jinsi gani utaweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Spika, Kinondoni tuna mtandao wa barabara za lami wa kilomita 165 na kwenye Jimbo langu barabara za lami ni kilomita 95.35 na hapa nataka nizungumzie kitu kinachoitwa spot maintenance ule ukarabati wa mashimo katika barabara. Eneo hili ni gray area Mheshimiwa Waziri Mkuu, linatisha.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka huu Serikali imetenga Shilingi Bilioni 5.6 kwa ajili ya kutengeneza mashimo. Najua Wabunge wengi waliomo humu ndani wanaishi Kinondoni au wanapita Kinondoni. Tuna barabara ambazo zinapata mashimo mara kwa mara, sasa fedha zinazotengwa ni fedha nyingi sana 5.6 billion Shillings ni hela nyingi sana kwa ajili ya kuziba mashimo.

Mheshimiwa Spika, kwa nini nalileta suala hili mbele yako na mbele ya Waziri Mkuu ni kwamba mashimo yale kila siku yanakuwa ni yale yale, huu ni mradi. Leo likitengenezwa shimo lile baada ya miezi mitatu litatengenezwa tena shimo lile lile. Huu ni mradi, kwa sababu fedha nyingi kama zile zinamalizika namna gani? Kwa viraka vidogo vidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka na naiomba Serikali kwanini isifikirie utaratibu wa kurudi kizamani angalau kwa majaribio katika Jiji la Dar es Salaam, tuna karakana kule Ilala, tuna karakana pale Mwananyamala pale Kinondoni, kwanini Serikali isitumie na kuwa na vifaa na mafundi wetu wa kutengeneza mashimo yale ili tukaondokana na huu utaratibu ambao sasa hivi watu wanatumia fedha nyingi kuziba mashimo yale yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfano upo mzuri sana, ukitembea Kinondoni utaona, ukiweka alama pale kuna barabara inaitwa Tarimba Road ambapo napita kila siku, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kila baada ya miezi mitatu, lazima itatengenezwa eneo lile lile, hivi hatuoni? Kwenye hilo, nitakuomba Mheshimiwa Waziri Mkuu ulisimamie, kwa sababu yawezekana tunaweza tuka-save fedha nyingi kwa utaratibu ambao nimeupendekeza, kwa sababu zamani ulikuwepo utaratibu huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alichukue hili aweze akalifanyie kazi ili aweze kuliangalia, si vibaya ukafanya utafiti cost benefit analysis kuweza kujua kama tukiendelea na utaratibu wa sasa hivi ama tukiendelea na utaratibu wa kuwa na karakana zetu kipi kitaifaidisha Serikali na kuweza kuipa thamani ya fedha kwenye maeneo haya. (Makofi)

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, taarifa!

SPIKA: Mheshimiwa Tarimba kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mpembenwe.

T A A R I F A

MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba anachokisema ni kitu sahihi kwa sababu hata pale katika barabara ya Msimbazi kuna wawakilishi ambao wanaiwakilisha nchi mashindano ya kimataifa, barabara pale siyo nzuri. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Tarimba, malizia mchango wako.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa sababu hii taarifa siwezi nikaipokea kwa sababu sijapita hiyo barabara bahati mbaya niko Kinondoni.

Mheshimiwa Spika, jingine ambalo ningeomba Mheshimiwa Waziri Mkuu tuliseme ni usimamizi wa miradi ambayo Serikali inawekeza fedha nyingi sana. Pale Kinondoni, kuna maeneo ambayo yanapata sana mafuriko wakati wa mvua. Kata za Dugumbi, Kata ya Tandale, Kata ya Makumbusho, Kata ya Magomeni, Kata ya Mwananyamala na Kata ya Hananasifu, kuna Mto ambao unaanzia Sinza kwa Mheshimiwa Profesa Kitila, ule mto unakuja unapita unaitwa Mto Ng’ombe.

Mheshimiwa Spika, Serikali mwaka 2019 ilipata Mkandarasi anaitwa CHICO kampuni moja ya Kichina, kwa thamani ya Shilingi Bilioni 32.5. mpaka tunavyozungumza mradi huu ulitakiwa umalizike mwaka 2019 ambapo ndiyo umeanza na umalizike Desemba, 2020.

Mheshimiwa Waziri Mkuu mradi huu haujamalizika, Mkandarasi hayupo katika eneo la kazi na ameshalipwa shilingi bilioni 20 kati ya zile Shilingi Bilioni 32. Kazi iliyofanyika ni asilimia 76 na ameongezewa muda mpaka mwaka jana tarehe 31 Desemba, 2021 bado hakuna kinachofanyika, mvua zinaweza zikaja, wananchi hawa wakaendelea kupata matatizo, ninaiomba Serikali iingilie kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haiyumkiniki Kinondoni mahali ambapo kuna watu wengi, mahali ambapo pana shughuli nyingi na wananchi wale wanaendelea kupata shida katika mafuriko wakati Serikali ilishatenga fedha na ilishalipa fedha asilimia zaidi ya 76.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Wananchi wa Kinondoni wameniambia, Serikali Sikivu kama hii na hasa wewe ambaye uko tayari kwenda kila mahali penye matatizo. Juzi ulikuwa Bukoba, kwenda kutatua matatizo ya kilimo ninakutarajia siku moja uibukie pale Kinondoni, ulione hili suala. Naamini kabisa ukionesha rangi yako tunayokujua, siyo rangi ile nyekundu hapana! Rangi yaani kwa maana your true colors za uchambaji kazi naamini kabisa wasimamizi wa miradi hii wataona naam! Sasa Serikali iko serious. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakuomba kwa sababu pale tulio wengi ni wacha Mungu, tukiomba dua mara nyingi Mwenyezi Mungu anasikia. Tunataka tukuombee Mungu katika eneo hili kwamba na ninyi mnuse nusu fainali, hebu tufanyie hii kazi. Mkitufanyia hii kazi sisi tutakwenda kukesha msikitini tarehe 17 Mwenyezi Mungu awajalie mambo yenu yawe mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, unajua mimi ni ‘Walii’ nikizungumza niko katika swaumu basi mambo haya Mwenyezi Mungu atakwenda kuwajalia, mimi ni mtu mwema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kukupongeza kwa mara nyingine pamoja na Serikali zima kwa kazi nzuri unayofanya na niwatakie kila la heri, Mwenyezi Mungu atujalie, kwa wale ambao wanafunga, Kwaresima Karim, basi Mungu awajalie kila jema na wale walio katika mfungo wa Ramadhani Mwenyezi Mungu awajalie. Hizo ndizo salamu kutoka Kinondoni, nawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuunga mkono hoja hii. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nikiwa mchangiaji wa kwanza jioni ya leo. Awali ya yote naomba nitamke kwamba Taarifa ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira pamoja na Kamati nyingine ya Kilimo, Ardhi na Maliasili taarifa zote hizo nazikubali na naziunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa nichangie upande wa Viwanda, Biashara na Mazingira na nimechagua maeneo hayo kutokana na ukweli kwamba nchi yetu au nchi yoyote ile ili ipate maendeleo ni hakika lazima iwe na uwezo mzuri sana wa kukusanya mapato yake na mapato ya nchi yoyote ile iwe ni upande wa kodi ama mapato ambayo si ya kikodi, lazima yawe yanatokana basi na shughuli ambazo ni za kibiashara, kilimo na viwanda. Sasa hii ndio sababu ambayo inanifanya niweze kuchangia katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nikiangalia mapato ya Serikali katika bajeti yetu hii ya mwaka 2022/2023, utaona kwamba tunakwenda kukusanya, makisio yetu ni trilioni 41.48 na kati ya hizo trilioni 23.65 zinatokana na kodi, hii ni sawa na 57%. Ukiangalia kiwango ambacho sisi tunakusanya na ukijaribu kukipima na pato la Taifa kuna ratio wanaangalia pale na inaonesha kwamba kodi ambazo sisi tuna uwezo wa kukusanya ni 11.7% ya pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda pengine kwa wenzetu ambao wanatusikiliza, uwiano huu maana yake ni nini? Uwiano huu ni zile fedha ambazo Serikali tunakuwa na uwezo wa kuzikusanya kutoka katika shughuli za kibiashara, fedha zinazozunguka kwa maana ya pato la Taifa na ni kipimo vilevile kuonesha ni jinsi kwa gani Serikali ina uwezo wa kukusanya kutokana na shughuli za kiuchumi. Tunajua kwamba hizo shughuli za kiuchumi tulizozizungumza ni kilimo, viwanda, ajira, biashara na vyote hivi katika asilimia kubwa sana ni shughuli ambazo zinafanywa na private sector.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia uwiano wa nchi nyingine hasa nchi zinazotuzunguka wenzetu wako vizuri, uwiano wa wastani unaotakiwa kukusanya fedha kutoka katika shughuli hizi za kiuchumi zisiwe chini ya 15% ili tuweze kukaa vizuri. Ndio maana unakuta tuna pengo kubwa sana katika bajeti yetu ambayo lazima tukope ama tutafute njia nyingine ya kujazia pale. Sasa kwa kuwa tunafahamu na Serikali yenyewe ilifahamu tangu mwaka 2015/2016 ikaamua kuja na kitu kinachoitwa blue- print kama mwarobaini wa kutuondolea matatizo yanayohusiana na ule ugumu wa kufanya biashara katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya nchi 190, Tanzania ni nchi ya 141. Sasa katika hali kama hiyo tunafanyaje biashara ili kuweza kupata fedha za kutosha na hapa ndipo ninapowaita viongozi wa Wizara hii kwamba kuna haja kubwa sana ya kuwa serious, I am sorry natumia hili neno kuwa serious, asubuhi kulikuwa na discussion ya Liganga na Mchuchuma hapa, contract ambayo imekuwa signed mwaka 2011.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu niambie kuanzia 2011 mpaka leo ni miaka mingapi? Miaka kumi na ushee bado tunaambiwa majadiliano hayajamalizika na hata Kamati, situmii neno imelalamika, lakini Kamati inasema haijaridhishwa na inaitaka Serikali iweze kuendelea na majadiliano kwa uharaka sana. Sasa hili neno ni la kisiasa mno, uharaka mimi kwangu linanipa mashaka, kwa sababu miaka kumi tayari imepita tangu mkataba umesainiwa. Uharaka ni mpaka lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ningeiomba Serikali, kwa kuwa kuna fedha nyingi pale katika machimbo haya ya makaa ya mawe, machimbo ya chuma na tunahitaji sana chuma katika shughuli zetu nyingi, ni uchumi mkubwa huo. Sasa leo kama tunaendelea kuambizana kwamba tuharakishe majadiliano hata kama tumeona matatizo. Ukisoma marejeo mengi sana ni kweli kuna matatizo, lakini hatuwezi kuendelea kukaa tukasema kuna matatizo na tukaambiana kwamba tuchepushe majadiliano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwamba Bunge hili lingeazimia vilevile katika taarifa hii kwamba Serikali ingepewa muda kama kuna uwezekano wa kuwapa muda, hata kama ni ndani ya mwaka mmoja, its ok, lakini ni ndani ya mwaka mmoja tuwe tumelipatia majawabu suala la Liganga na Mchuchuma. Hatuwezi kuendelea kulikalia kimya na tukafikiri kwamba all is well, all is not well kwa sababu hatuwezi tukaacha mali ikae ardhini na tuna watu ambao wangeweza kufanya uwekezaji, si lazima mwekezaji yule, lakini tufikie mahali tufanye maamuzi basi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafanikio ya ufanyaji biashara, nimezungumza yanategemea na urahisi na uzuri wa ufanyaji biashara. Nataka nitumie tena neno lingine seriousness ambayo inatakiwa ionyeshwe kwenye Serikali hii ambayo ni sikivu kwamba yawezekana vipi tutunge blue-print sisi wenyewe na Serikali ikaweka mkono wake pale, lakini ishindwe kutekeleza blue-print. Wana sababu gani kwa Serikali kushindwa kutekeleza blue print? Ingekuwa ni document imeandikwa na watu wengine, wakaletewa wao kwa ajili ya implementation, tungeweza kusema kuna mambo mle ndani hayafai, lakini ni mambo ambayo yametengenezwa na Serikali yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba na ningeshauri Bunge hili lije na maazimio kwamba, Bunge linaazimia kuwa Serikali ije na mpango mahususi wa utekelezaji wa blue print katika maeneo ambayo yataondoa ukiritimba uliopo katika regulators, ni ngumu sana kufanya biashara sasa hivi nchini kwetu. Najua kuna dhamira nzuri sana ya Serikali waliionesha kwenye Bunge lililopita karibu sheria 15 zilifanyiwa marekebisho, lakini marekebisho yale si yenye kushika moyo kabisa wa wafanyabiashara, ni marekebisho ya juu juu. Ningependa Serikali ije na kauli kwamba kweli inakwenda kudhamiria na kama ikiwezekana ituletee ripoti ituonyeshe status ya utekelezaji wa blue print imefikiwa namna gani? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie upande wa umeme. Bila ya umeme, najua kuna juhudi za Serikali, tunakwenda kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere, lakini hali ilivyo sasa hivi kule kwetu Dar es Salaam ni shida. Ni shida kwa sababu sisi hatuna mashamba, sisi hatuna REA, sisi hatuna labda kilimo, pale Kinondoni tunafanya shughuli za vibiashara vidogo vidogo na kushughulika na viwanda vidogovidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ambayo yana shida ya umeme ya kukatika kila mara, naomba nikutajie, pale Kinondoni mjini penyewe, Hananasifu, Magomeni, Mzimuni, Kigogo, Mwananyamala, Tandale, Kijitonyama, Makumbusho na Kata ya Ndugumbi, ni maeneo ambayo haipiti siku lazima umeme ukatike. Unafanya vipi biashara katika hali kama hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kuna Wizara inahusika na masuala ya nishati, lakini Serikali yenyewe izungumze. Hapa siku zote tunasema mifumo katika Serikali haizungumzi, mifumo ya kodi izungumze. Sasa kama mifumo yenyewe haizungumzi, kwa nini Serikali haitaki kuzungumza? Izungumze kati ya Wizara na Wizara kwa sababu hakuna Wizara moja inaweza ikasimama peke yake, kila Wizara inamhitaji mwenzake. Kwa hali hiyo tunapozungumzia suala la biashara, tunapozungumza suala la viwanda lazima viende pamoja na masuala ya utoaji wa huduma ya umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi uliyonipa. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie nikiwa mchangiaji wa mwisho na ninajua mara nyingi mchangiaji wa mwisho hutampigia kengele utamuachia tu atiririke wee! mpaka amalize. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Bajeti na ningependa nizungumzie masuala ambayo yamewasilishwa na Mwenyekiti wetu, haraka niseme naunga mkono hoja zote mbili kwamba mimi kwangu ni asilimia mia moja kwa mia moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ni mpenzi wa kusoma sana hizi Journals za mambo ya kiuchumi, hivi karibuni nikasoma jarida moja linaitwa Africa can end poverty wakiwa na maana kwamba Afrika inaweza ikaondokana na umaskini, pale nikavutiwa na andiko moja la Ndugu mmoja anaitwa Waly Wane huyu ni Daktari wa Uchumi katika taasisi moja inaitwa Development Research Group. Huyu aliandika akajiuliza swali is Tanzania raising enough tax revenue? Alikuwa anajiuliza yeye katika thesis aliyokuwa anaandika kwamba hivi Tanzania inakusanya kweli kwa uhakikia kodi inayotosha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ni andiko la siku nyingi kidogo la tarehe 4 Februari, 2013. Sasa katika kusoma kwangu nikasema ngoja nifananishe na hali halisi hapa kwetu. Nichukue kwanza nafasi kusema kweli ya kuipongeza Serikali kwa maana ya TRA kwa maana mwaka 2021/2022 mapato ya ndani Serikali imeweza kukusanya trilioni 24.35 dhidi ya lengo la trilioni 25.6 na hii ni sawa na asilimia 95 Kamati imetoa pongezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizi na juhudi kubwa iliyofanywa hawa akina Ndugu Waly Wane swali lao bado halijajibiwa. Nimejaribu kuangalia pia mapato yetu na mienendo ya jinsi tunavyofanya mipango yetu swali la Waly Wane bado halijajibiwa. Sasa nikasema hebu niangalie Kamati imeliangalia vipi suala hili, kwa mujibu wa maelezo ya Kamati kama ilivyo katika paragraph 2.1.7 kuanzia ukurasa wa kumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa sijui nilijibu hili swali ama Bunge litajibu lakini tusikilize Kamati inasema nini, na maneno haya aliyasema hata Mheshimiwa Esther, kwamba kuna baadhi ya wafanyabiashara wasio waaminifu hawatumii machine za EFD, maana yake ni kwamba kuna upotevu hatukusanyi, kumbe sasa swali la Ndugu Waly Wane tunaanza kuliona kwamba kweli alivyouliza ni kwamba kweli hatukusanyi inavyopasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuangalie jambo la pili baadhi ya Halmashauri zetu haziwasilishi fedha benki, hizo fedha zinakwenda wapi kama haziwasilishwi benki maana yake zinapotea, hazikusanywi na Serikali maana yake jibu ni kwamba hatuzikusanyi Serikali haipati mapato yake. Hata ukija kwenye masuala ya fedha ambazo hazikusanywi kutokana na madeni ambayo yamelimbikizwa, hilo nalo ni suala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda kwenye idadi ya watu ambao wameandikishwa walipa kodi, watu Milioni Nne ndiyo wako katika kanzi data, watu wanaolipa ni nusu yao maana yake hata Mheshimiwa Esther aliuliza je, kama hao wengine Milioni Mbili waliobaki wangekuwa wanalipa tungekuwa tunapata kiasi gani? Hilo nalo ni swali la Ndugu Waly Wane anauliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye masuala mengine ya watu wanao file returns - marejesho ya kodi kwa njia ya ki- electronic, wapo watu ambao wameonekana hawafanyi hivyo maana yake hatuzikusanyi fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tax audit ambazo zinachelewa, hili tumelisema hapa Bungeni, inachukua miaka mitatu, minne kwa TRA kwenda kufanya tax audit, fedha za Serikali zimekaa pale hatuzikusanyi, na hilo nalo ni suala vilevile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuchelewa kuanzishwa kwa Ofisi ya Msuluhishi wa Kodi ambapo pengine masuala ya Kikodi yasingekwenda TRAB na TRAT kule yangeweza kusuluhishwa lakini bado haijamalizika. Hata haya mashauri yaliko katika hizi mahakama za TRAB na TRAT hazina muda. Zinaweza zikakaa muda wote ule, hakuna specific period kwamba ikifika muda fulani mashauri yamalizike, Serikali ipate fedha zake au mfanyabiashara arudishiwe fedha zake. Haya ni mambo ambayo tungependa tuyaone kwamba ni concern kubwa kwamba ni vitu vinavyotugusa. Kwamba laiti kama vitu hivi vitafanyika kwamba ni dhahiri kabisa inaweza tukapata fedha za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu tuangalie kule Mtaa wa Nyamwezi pale Dar Es Salaam, ambao umejaa maduka mengi sana. Pale wale Maafisa wa Kodi ambao wanasimia ile block wapo Maafisa Watano tu na mtaa ule mpaka wakiumaliza kuutembelea maana yake watahitaji hata mwaka mzima. Yawezekana kuna wafanyabiashara wengine hata hawapitiwi kabisa kuweza kupeleka taarifa zo za kikodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti,ni kisema hivyo maana yake kilio cha kupatikana kwa wafanyakazi wa kutosha wa TRA bado kiko pale pale, tusipokuwa na wafanyakazi wa kutosha TRA hatuwezi tukakusanya ela. Najua Serikali imejitahidi sana kuongeza idadi ya Wafanyakazi wa TRA lakini hakika hiyo inaanifanya nifikirie jambo moja. Kule kwenye Kata zetu, kila kata kuna Afisa Maendeleo, kila kata kuna Afisa Ugani, Kuna Afisa Elimu tunashindwa nini kuweka kila kata Afisa wa kodi. Tunaona taabu ya nini tuanze na Dar es Salaam tuangalie yale maeneo ambayo yanashughuli za kiuchumi nyingi ili tuweze kuwakia wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais aliyepita Mheshimiwa Jakaya anasema maneno haya ni very famous anasema kama huwezi kuliwa huwezi kula, ukitaka kula lazima uliwe, sasa sisi tena hawali watu wabaya wanakula watu wetu, Watanzania wakiajiriwa watatusaidia kukusanya kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,hili linanipeleka vilevile kwenye utaratibu mwingine, naomba Serikali iweke katika mitaala yake hata kuanzia primary school, somo la uzalendo na ulipaji wa kodi. Watu wetu wakue wakiwa wanajua umuhimu wa uzalendo na umuhimu wa kulipa kodi. Hii pia itatusaidia kwa sababu kama tunatafuta fedha za kutosha na huku tunajua fedha za kutosha zinatoka katika private sectors, private sector kwa maana ni biashara, leo kulikuwa na swali linaulizwa hapa linahusiana na blueprint tuko nchi ya 141 na hili nalisema sana mwisho nitapewa jina la blueprint. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuko 141 Serikali inaulizwa lini mtatuletea taarifa ya utekelezaji, majibu yanayoletwa hapa yaani saa nyingine tunaheshimu Serikali yetu lakini saa nyingine unashangaa unaweza ukasema ni ya kisiasa mno! Tunataka taarifa zile za kufanya ufanyaji wa biashara Tanzania uwe mwepesi, watu waweze kutupatia kodi, sasa hilo pia nalo lina ugumu gani? Haya mambo mengine unayazungumza na mimi kwa sababu hili eneo la fedha ni la Ndugu yangu Mwigulu, najua ni mwananchi mwenzangu, yaani najizuia kwelikweli kutumia maneno mengine yasiyofaa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tarimba nilikuongeza dakika kidogo lakini nadhani tumefika mwisho.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Haya ahsante.

MWENYEKITI: Nakushukuru kwa mchango wako.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niwe Mbunge wa kwanza kuchangia katika hoja hii ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani Engineer Masauni. Mimi mchango wangu ningependa zaidi nijikite katika lile suala linalohusiana na hali ya usalama barabarani kama ilivyo katika ukurasa wa 15 na 16.

Mheshimiwa Spika, suala hili limenifanya nichangie kwa sababu nilikuwa nikiangalia takwimu ambazo Mheshimiwa Waziri amezileta si takwimu nzuri. Hii ni kwa sababu kumekuwepo na ongezeko, vifo pamoja na ongezeko la majeruhi ya wananchi ambao sisi tunawawakilisha humu Bungeni. Nikiangalia, sisi Kinondoni kwa mwaka 2020 tumeonekana kuongoza. Idadi yetu ya watu ambao waliopata ajali ni ajali 353 ni kubwa kuliko wilaya nyingine ama mkoa mwingine wowote.

Mheshimiwa Spika, hii ni hatari hasa ukiangalia kwamba wanaoumia sana sana ni vijana wetu na watu wetu ambao wanaishi katika maisha ambayo lawlessness kama wanavyowaita Waingereza, hasa ukiangalia pale Dar es Salaam. Sasa vitu kama hivi haviwezi vikaendelea kuwepo. Na hata ukiangalia Mheshimiwa Waziri mwenyewe anakubali kwamba ajali zinaongezeka.

Mheshimiwa Spika, ajali zinaongezeka ukiangalia takwimu; hivyo na mimi ningependa nijielekeze hasa kuhusu hawa waendesha boda boda; na ninapenda Waheshimiwa Wabunge wasifikiri kwamba mimi ninapiga vita biashara ya boda boda, hapana, napenda biashara ya boda boda iendelee, lakini ningependa iendelee kwa kufuata kanuni na sheria tulizojipangia. Sheria hizi ni kama ile Sheria ya Law Traffic Act ya Mwaka 1973.

Mheshimiwa Spika, nimefanya utafiti na nimezunguka sana, nimekwenda kwenye Taasisi yetu ya Takwimu (National Bureau of Statistics), nimekwenda traffic Makao Makuu nimepata taarifa, lakini vile vile nimekwenda kwenye hospitali yetu ya Mwananyamala kuangalia idadi ya watu ambao wanapata ajali. Sasa, leo nikaja nikashangaa nilivyoona takwimu nyingine inayotolewa na Wizara. Hakika haya maeneo yote ambayo ni maeneo ya Serikali, mifumo ya utoaji wa tarakimu ni matatizo Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Spika, takwimu hazioani hata. Ukiangalia takwimu zinavyoonyesha ni kwamba watu wa Bureau of Statistics wao wanasema kwa kutoa mfano, kwamba kwa mwaka 2020 taasisi inasema ajali za pikipiki zilizotokea nchini zilikuwa 505. Lakini ukienda Traffic kwenyewe wanakwambia 404 na hizo karatasi ninazo. ukiangalia hata takwimu za vifo haziendani.

Mheshimiwa Spika, ningeshauri kwamba Serikali ije na mfumo wa kupata takwimu zake sahihi ambazo zitakuwa relied upon, tutazitegemea. Kwa sababu bila ya kuwa takwimu sahihi unaendaje kutafuta solution, unakwendaje kutafuta majawabu kwenye matatizo ambayo sasa hivi yanaonekana kuongezeka. Hilo ni jambo langu la kwanza, ningemuomba Mheshimiwa Waziri aweze kuliangalia.

Mheshimiwa Spika, lakini kingine ambacho kimenishangaza kidogo ni pale ninavyoona takwimu za piki piki Kinondoni ajali 64. Nikiangalia, mimi ninakaa Kinondoni na ninavyotembea mule haipiti siku mbili au tatu utakuta mtu kagongwa na kuna mwingine amefariki; lakini takwimu itakwambia 64. Ina maana kila baada ya siku sita ama wiki ndiyo ajali moja inakuwa reported. Haiwezekani kwa mji kama Kinondoni ambayo ina kilomita 1,663 na piki piki ziko nyingi kiasi kwamba ukiendesha gari Kinondoni; na maeneo mengine hata hapa Dodoma; utashangaa kuona kwamba kuna matatizo makubwa. Kwa mfano, kupita taa nyekundu ni kitu cha kawaida, kwenda no entry ni kitu cha kawaida, kujaza abiria; piki piki inatakiwa iwe na mtu mmoja kwa mujibu wa Sheria lakini; wanakuwepo watu zaidi ya wawili kwa maana ya mishikaki, mjini tunaita mishikaki natoa mfano tu, hiyo yote inakatazwa katika hii Sheria. Lakini utafiti wangu nilioufanya kule traffic wanasema...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia mchango wako.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nilifikiri dakika kumi. Anyway, ninachoomba cha msingi ni kwamba Mheshimiwa Waziri aharakishe ule Muswada ambao mnataka kuuleta kwa minajili ya kufanya marekebisho katika Sheria ya Road Traffic ya Mwaka 1973, iharakisheni. Kwa sababu huo Muswada nimeuona, upo, basi uharakisheni kwa sababu hata adhabu zinazotolewa hazitoshelezi. Tumepunguza adhabu ya shilingi 10,000 hapa, adhabu hii inafanya watu waendelee kufanya makosa. Naomba Serikali ifikirie upya adhabu ambazo zinaweza zikatumika ili kuweza kuwa deterrent…

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nakushukuru.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Nimpongeze Profesa Mkenda kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Nitazungumzia eneo moja tu, eneo linalohusiana na tafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikiangalia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameizungumza vizuri sana katika ukurasa wa 11, lakini vile vile akasherehesha katika ukurasa wa 66. Nampongeza na naipongeza Wizara kwamba imevuka malengo yake katika idadi ya tafiti ambazo ilikuwa imejipangia, tafiti 129 lakini wakaenda kufanya tafiti 143.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nianze mchango wangu kwa kumwangalia Mwanafalsafa mmoja, aliishi miaka mingi sana. Huyu bwana alikuwa na umri wa miaka 70 na aliyazungumza maneno fulani hivi kati ya mwaka 1072 alipozaliwa, yeye alifariki mwaka 1142. Yeye anasema nini katika upande wa utafiti. Anasema na naomba nitumie lugha ya Kiingereza:

“The world will come to prove the researches shall become a crucial factor to moving the world to prosperity”.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa alikuwa anasema, dunia itakuja kuthibitika au kuthibitisha kwamba tafiti ndizo zitakuwa ni majawabu katika kuondoa au kutafuta hali njema za watu duniani na maendeleo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikajaribu tena kwenda mbele zaidi, kuna msomi mmoja kutoka Ugiriki, huyu anaitwa Atanasis Valevanidis kutoka Chuo Kikuu cha Athens kinachoitwa National and Kapodistrian. Huyu bwana anasema nini? Huyu bwana naye alifanya utafiti juu ya nafasi ya Vyuo Vikuu katika kufanya tafiti zinazotafuta majawabu ya maisha ya watu katika nchi zao na maendeleo yao. Hivyo anathibitisha na kusema

“Dunia sasa imekubaliana kuwa research and development kuwa ni nyenzo muhimu sana katika kuipeleka nchi yoyote including Tanzania, nchi yoyote katika kutafuta majawabu ya matatizo yao”.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaona ni kwa jinsi gani vyuo vikuu vimekuwa ni chanzo kikubwa sana cha ufanyaji wa tafiti. Sasa hapa kuna swali moja ambalo napenda kujiuliza.

Ukiangalia katika Vyuo Vikuu vya nje ambavyo nitatoa mfano, Chuo Kikuu cha Manchester; Chuo Kikuu cha Manchester ni moja katika vyuo vikuu ambavyo vinajisifu sana, vinajitanua sana, katika masuala ya research; wenyewe wameshafanya research za maji salama kwa watu maskini kama sisi kwenye nchi zinazoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, researches zile zikifanyika zinakwenda kuwa-commercialized lakini vilevile zinakwenda kutumiwa. Wamefanya research nyingi sana. swali linalokuja ni kwamba sisi hapa tunapopata matatizo Vyuo Vikuu vyetu vinatutoa katika matatizo? Tulipata hapa matatizo ya Corona, kama siyo kama Mheshimiwa Shekilindi kutusaidia, vyuo vikuu vyetu vilikuwa vimekaa tu kimya ukiondoa COSTECH nafikiri walifanya kazi fulani hivi. Sasa ninapojaribu kusema, nataka hili nimuulize Profesa, wakati akihitimisha; nimeangalia University of Dar es Salaam hakika wanafanya kazi kubwa sana, lazima tuwapongeze. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda katika site yao pale wanakuonesha ni jinsi gani research muhimu sana za kisomi, zinazotafuta majawabu katika matatizo tuliyonayo; matatizo ya kisayansi, kilimo, energy na ya kimaskini, lakini najiuliza ni research ngapi Mheshimiwa Profesa Mkenda wanakwenda kuzitumia? Ni ngapi zinatumiwa au zimebakia katika shelves? Ukichukua hata zile za undergraduates, wengine wanakuja na topics za maana kabisa. Je, kuna extension zozote zile za research ambazo zinafanywa au watu wakishafanya research zimewekwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia moja ya kazi ya Wizara hii kubwa kabisa ni tafiti; wenyewe hii ni katika moja ya kazi zao na ni kazi ya kwanza. Ningependa Tanzania hii, iweze kuthamini masuala ya researches, lakini vile vile Serikali iweze kupanga fedha za kutosha kuweza kufanya tafiti hizi. Ndiyo maana baadhi ya maamuzi yetu yanakwenda kuwa na matatizo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, researches hizi zitatusaidia hata policy makers kujua wanatengeza policy za aina gani, sera za aina gani kuisaidia nchi. Bila ya kufanya tafiti tunaweza tukakuta, kama tulivyofanya wakati Fulani, silipendi jambo hili lakini nalisema kwa sababu ya uchungu, tuliuza nyumba za Serikali, si mnakumbuka? Tuliuza nyumba za Serikali, tulifanya tafiti kweli kwamba kile kitendo cha kuuza nyumba za Serikali kilikuwa na manufaa kwa Taifa hili? Utafiti ungekuwa umefanyika mapema na ukatoa majawabu kwamba kuuza nyumba za Serikali kuna faida, hakika ingeweza kutusaidia kujua tunachokifanya kinatusaidia ama hakitusaidii.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme kwamba naunga mkono hoja hii, lakini nitafurahi sana kumsikia Profesa akileta majawabu ya aina ya tafiti zilizofanywa Tanzania na zile ambazo zimeweza kuisaidia nchi hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia Hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Awali ya yote nipende kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba nzuri, hotuba ambayo inaonesha ni kwa jinsi gani Serikali yetu imepiga hatua katika kuleta maendeleo lakini vile vile kuweza kuwasaidia wananchi wake kupata uhuru wa kutosha wa kiuchumi na masuala mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na vile vile nisimame hapa kwa niaba ya Jimbo la Kinondoni na wananchi wa Jimbo la Kinondoni niweze kumshukuru sana na kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa yale ambayo ametufanyia sisi wananchi wa Kinondoni. Kinondoni tumepata maendeleo makubwa sana ndani ya kipindi cha miaka miwili. Naamini wengi mlioko humu ndani katika Bunge hili mnaishi au mna ndugu pale Kinondoni; na kwa hali hiyo mnapita na mnaona ni jinsi gani Kinondoni imechangamka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe mfano maeneo mawili au matatu. Kwa mfano kwenye Kata ya Kinondoni ambapo ndiyo kata iliyochukua jina la Jimbo na jina la Wilaya; kata ile katika miaka 60 ya uhuru wetu haijawahi kuwa na secondary school ya Serikali lakini safari hii tumepata secondary school ya Serikali ya kisasa na watoto wameshaanza kusoma. Vilevile pale hatujawahi kuwa na kituo cha afya wala dispensary. Kinondoni sasa hivi ina kituo cha afya cha kisasa ambacho kimejengwa na Serikali na kinapendeza na kina huduma zote, nipende kuishukuru Serikali kwa ajili hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kuna barabara nyingi ambazo zimejengwa katika kata ile ikiwemo barabara ya Best Bite ambayo kwa miaka nenda miaka rudi ilikuwa ni kero sana. Pia nishukuru Serikali kwenye zile Bilioni moja ambazo Mheshimiwa Rais alizitoa kwa kila Mbunge kwa minajili ya kujenga barabara katika majimbo yetu mimi nimeipeleka kwenye kata moja ambayo ilikuwa haina barabara za lami hasa kata ya Ndugundi tumepata barabara mbili, Mkalamo moja na Mkalamo mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti,vile vile nishukuru Serikali kwa kuangalia suala la mafuriko katika Jimbo la Kinondoni. Mto Ng’ombe umekamilika, na hata mvua za juzi tulikuwa salama sana. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu ambaye tulikuwa naye kule kwenda kuangalia, na maelekezo aliyoyatoa yametekelezwa, hivyo hongera sana kwa Serikali kwa kutufanyia jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna suala la Mto Msimbazi, tumelizungumza sana. Napenda nitoe pongezi nyingine kwa Serikali kwamba sasa mradi ule wa kuboresha eneo lile la Bonde la Mto Msimbazi unakwenda kufanya kazi; na tayari tathmini zimefanyika na hivi ninavyozungumza jumla ya nyumba 2,592 zilifanyiwa tathimi na katika nyumba hizo 2,217 wamekubaliana tathmini zile. Isipokuwa nyumba 163 wenye hizo hawajakubaliana na tathmini.

Nilikuwa naiomba Serikali kwa utaratibu uliopo wa Kiserikali uendelee kufanya mazungumzo na wananchi hawa ili nyumba zao ziweze kufanyiwa upya marejeo ya tathmini ili waweze kupata tathmini ambayo inakubaliana na thamani ya nyumba zao ili mradi ule uweze ukaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mafanikio yote haya kuna matatizo kidogo ambayo ningependa niyaseme. Kwa mfano kwenye Kata ya Kigogo tuna kituo cha afya kikubwa sana ambacho kina hudumia wananchi wa Ubungo na wananchi wa Ilala. Kituo kile kilipelekewa jokofu la kutunza maiti mwaka 2020; na jana wakati nazungumza kuuliza swali la nyongeza kwa Wizara ya TAMISEMI nilikuwa naiomba Serikali iweze kufanya haraka kulipa fidia ili jingo la kuhifadhi mashine ile ya jokofu la maiti iweze kujengwa na Serikali ikasema na ikaagiza halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni waweze kutenga fedha za kujenga jengo la kuhifadhi jokofu la kutunzia maiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ajabu ni kwamba kumbe wakati mimi namaliza kuzungumza lile jokofu limekwenda kuondolewa limepelekwa kwenye Hospitali ya Wilaya Mabwepande. Hiyo hali sikuipenda sana kwa sababu kumbe Waziri ana taarifa nyingine, TAMISEMI kwa maana ya watendaji wana taarifa nyingine, hili jambo si zuri na halioneshi kwamba Serikali ni moja na inafanya kazi kwa pamoja. Huyu anafanya maamuzi yake na huyu mwingine anafanya maamuzi yake, hawaambizani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili si jambo jema kwa utendaji wa Serikali ambayo ina sifa nzuri ya kuweza kuwatumikia wananchi wake. Nitaomba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI au Naibu wake niende naye kwenye Kata ya Kigogo ili aweze kuona jinsi gani hali ile ambayo imefanyika sasa hivi inakwenda kuathiri wananchi. Hii ni hatari kwa sababu maelekezo mengi ambayo yanatolewa hapa Bungeni wananchi wanayachukulia kwa ukubwa wake lakini sasa kama Waziri anasema fedha zitengwe na wakati huo huo mamlaka nyingine zinakwenda kuondoa jokofu maana yake kama vile kuna crush kati ya Serikali kuu na Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba na mimi nigusie suala hili ambalo linatula vichwa vyetu. Sisi Wabunge ili uwe Mbunge lazima ule kiapo; na katika kula kiapo lazima utashika ima Biblia takatifu ama Quran takatifu. Asubuhi kila tunapoanza shughuli za Bunge tunaomba dua na tunamtaja Mwenyezi Mungu hapa na tunamwomba atupe hekima kufanya maamuzi na kufanya mambo mengine. Lakini Mungu huyu tunamchukiza. Mungu huyo huyo ambaye tunamsema kwamba ndiye kiongozi ambaye anatuongoza sisi katika maisha yetu tunamchukiza. Tunamchukiza kivipi? Matendo tunayoyazungumza ya kiushoga ni matendo yanayo mchukuza Mungu. Tumesema kama Bunge; na wananchi huko nje na viongozi wa kidini wanalalamika. Leo asubuhi kwa Waziri wa Elimu kulikuwa na swali ambalo lilikuwa linahusiana na masuala haya ya watoto kuharibika wakiwa boarding school, na Mheshimiwa mbunge mmoja alisimama akaomba kwamba je, Serikali haioni uharaka na umuhimu wa kuleta sheria mahsusi? Waziri anajiuma uma anasema watalichukua hilo wazo watakwenda kulifanyia kazi, alah! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unachukua wazo ambalo vitu vinaumiza vichwa vya watu. Jambo hili si la leo, mwaka 1998 kulikuwepo na sheria ambayo ilitungwa inasema Sexual Offenses (Special Provisions) Act, 1998 maana yake mambo haya yalikuwepo miaka mingi yanasumbua, yalikuwa ni madogo madogo. Hata hivyo Sheria ile haikuja explicitly, haiko kwa uwazi kabisa jinsi gani ya kuweza kupiga vita vitendo hivi, ingawa muda…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE.TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie maana yake hoja itakuwa ina-hang. Naomba kama haiwezekani kuleta sheria mpya hapa basi ifumuliwe Sheria ya SOSPA ya 1998 ili iweze ikakidhi mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi. Moja kwa moja kwanza, nimuombe Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aendelee kukubariki.

Mheshimiwa Spika, nataka kwanza nimpongeze Wakili, Mheshimiwa Angellah Kairuki, kwa kuja na hotuba nzuri sana ambayo inabeba na kuakisi maono ya Mheshimiwa Rais. Maono ambayo anataka maendeleo ya haraka. Hiyo katika hii miaka mwili ametuonesha, hivyo, mwaka huu wa tatu ambao tunakwenda nao sasa hivi Mheshimiwa Kairuki anaomba zaidi ya trilioni tisa katika bajeti yake. Naliomba Bunge hili liridhie kwa haraka sana ili tuweze kumpa nyenzo Mheshimiwa Waziri akafanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, nataka nizungumzie masuala yanayohusiana na kupata hayo maendeleo ya haraka, kwamba lazima tufanye kazi kwa bidii sana. Hapa napenda ninukuu maneno ya CAG Mstaafu, Alhaj Mussa Assad katika mchango wangu. Yeye alikuwa anazungumzia mambo gani muhimu ya kuyafanya ili tuweze kupata maendeleo ya haraka na akasisitiza katika kufanya kazi kwa bidii. Anasema siku zako mbili zisiwe zinafanana. Maana yake unachokifanya leo, kesho kifanye bora zaidi. Hili ndilo tunaloliona kwa Mheshimiwa Rais, kwamba kila siku yeye analokuja na jambo lake moja, siku ya pili linakuwa ni jambo zuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa natazama nione hata wasaidizi wake, yasiwe ni masuala ya kila siku sawasawa na siku nyingine. Tunataka maendeleo ya haraka na kwa kutaka maendeleo ya haraka maana yake ni kwamba kila siku tunachokifanya tunakiboresha kuliko jana yake.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni quantum of work, kwamba tuwe na muda mwingi sana wa kufanya kazi. Siyo kila siku tunafanya kazi kwa kipindi kilekile tu, kwamba kuna kazi nyingine hazisubiri muda. Ndiyo maana unaweza ukashangaa viongozi wetu hawa, mfano Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais, hata Mheshimiwa Angellah, unaweza ukazungumza naye saa 8.00 za usiku anaku-text, kwa maana huyo mtu anafanya kazi hata saa 8.00 za usiku. Hao ndio viongozi tunaowataka na hata kule chini kwenye halmashauri tukutane na viongozi wa sampuli hiyo. Siyo kiongozi ikifika saa fulani, saa 8.00, saa 9.00 anafunga mafaili anaondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, excellence. Kazi ambayo unaifanya lazima ujipime wewe, inakuwa bora kiasi gani, siyo bora kazi, kazi bora. Ndiyo viongozi tunaowataka. Sasa hayo unayakuta kwa Mheshimiwa Rais. Kila siku na kila Mbunge hapa akisimama anampongeza Mheshimiwa Rais, tunayataka haya yarudi kule chini, viongozi wa chini wamfanye Rais kama role model wao.

Mheshimiwa Spika, hili nalizungumza najaribu kuliangalia sana pale kwangu Kinondoni. Pale Kinondoni wakati nimepokea fedha za mwaka jana za Mfuko wa Jimbo. Mfuko wa Jimbo ule tukasema tukajenge eneo ambalo litatoa huduma za mama na mtoto, jengo la huduma ya mama na mtoto.

Mheshimiwa Spika, pale kulikuwa na eneo la wazi, watu wakilitumia kama soko. Wananchi wale nikishirikiana na Mheshimiwa Diwani wa pale ambaye anaitwa Mheshimiwa Mgana, tukaenda tukazungumza na wananchi wa pale kwamba ndugu zangu tunataka tujenge jengo kwa minajili ya kuwahudumia akinamama na watoto, tumepata fedha katika Mfuko wa Jimbo. Wananchi wale wakakubali kuhama eneo lile ili tuweze kujenga.

Mheshimiwa Spika, yote haya yanafanyika tukiwa na Viongozi wa Manispaa ya Kinondoni, wanaridhia. Baada ya kuridhia hata fedha zikahamishwa kutoka katika Mfuko wa Manispaa kupelekwa kwenye Ofisi ya Mtendaji wa Kata. Ajabu, baada ya muda kuna kiongozi, sitaki nimtaje kwa sababu hayuko hapa na hawezi akajitetea, lakini nitamwambia Waziri ni nani, anakwenda kule anafanya juhudi jengo lile lisijengwe. Kigogo ni eneo ambalo watu wengi sana pale ni maskini, hali zao ni za chini. Tunapowapelekea huduma kama zile tunawasaidia, lakini huyu mtu anaamua kudhoofisha juhudi za Mbunge, nasikia anataka kugombea Ubunge, nashangaa! Hugombei Ubunge kwa kuwaumiza wananchi. Kama unataka kushindana na Tarimba Abbas, come to me, usiwachezee watu. Wale watu wana matumaini yao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hebu angalia lingine, Tandale…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya, Mheshimiwa Tarimba, kengele ya pili imegonga, muda wetu umekwisha.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, lakini mfano mmoja unatosha, nawaomba tuipitishe hoja hii kwa nguvu sana. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa nafasi hii, na mimi naomba moja kwa moja nianze kwa kuunga mkono hotuba hii na niwashauri Waheshimiwa Wabunge tuipitishe hii bajeti bila ya ukakasi lakini bajeti hii lazima iboreshwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kwenda katika mchango wangu rasmi ningempongeza kwanza Mheshimiwa Rais ana maono mazuri sana, ana ndoto nzuri sana ametueleza jana wakati tulivyokuwa katika hafla ile ya kuipongeza klabu kubwa kabisa yenye historia kubwa katika nchi hii klabu ya Yanga ambayo imeshakuwa mabingwa sasa mara 29 wanakwenda kutawazwa leo jioni hii kuwa mabingwa wa 29 katika Premier League. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais amejipambanua kutaka masuala ya michezo utamaduni, yaweze kupewa kipaumbele stahiki na ameona kwa kupitia sports diplomacy kwamba kumbe Tanzania inaweza ikapata recognition ikatambuliwa nchi za nje kupitia michezo na nimefurahi sana tuliupokuwa kule Algiers Mheshimiwa Waziri alipata nafasi ya kuweza kukutana na wenzake wa pale Algiers, Algeria Mawaziri wenzake kuizungumzia habari ya Tanzania na michezo. Vilevile nimeona seriousness ya Serikali katika kupeleka mawaziri wawili, Waziri wa Serikali ya Muungano lakini Waziri Mwita kutoka Zanzibar. Hii inaonesha kabisa dhamira ya Mheshimiwa Rais kupeleka nguvu ya kutosha katika michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakuchukizwa na jambo la kupeleka bajeti ndogo. Mwaka jana tumepeleka billion 35.4, mwaka huu tunaomba tena 35.4 haya maono ya Rais yatafikiwa vipi? Ndoto ya Rais inafikiwa vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi hata siku moja na hata ukiangalia dhima ya Wizara. Dhima ya Wizara ni kukuza kuwezesha na kuendeleza utambulisho wa Taifa, maadili ya kiutamaduni, sanaa na michezo na wenyewe wakasema kabisa ili wafikie malengo haya lazima wawafikie wadau wafanye mageuzi kwenye taasisi wafanye utawala bora na uendelezaji wa miundombinu ya michezo huwezi ukafanya mambo hayo kwa bajeti hii tutakuwa tunataniana humu ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na Wabunge wengi waliozungumza kuhusu bajeti, lakini vile vile kamati imesisitiza suala la bajeti. Sasa kwa nini sasa Bunge lako hili lisiichukue hoja hii kama hoja mahususi ikapelekwa mbele ya Kamati ya bajeti ili Kamati ya bajeti itakapofanya majumuisho na kujadiliana na Serikali suala la kuongeza bajeti likawa ni moja kati ya mambo yaliyoibuliwa kutokana na mijadala hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba kwa kuwa michezo ya kubahatisha kwa sehemu kubwa sana inategemea sports, inategemea michezo. Iwe kwenye betting ama kwenye casino au michezo mingine kutokana na hili nataka nikupe figures hadi Mei 2023 hadi Mwezi uliopita, Serikali imekusanya bilioni 146.9 na imevuka malengo ya kukusanya bilioni 131.5 sasa kwa fedha zote hizi zinatokana na sports unapelekaje 35.4? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hayo mambo hayaendi na kwa hali hiyo, napendekeza suala la michezo ya kubahatisha iwe chini ya Wizara ya Michezo nafikiri ni suala muafaka. Yawezekana tumechelewa lakini Serikali ilichukue suala hili, michezo hii ipelekwe chini ya Wizara ili fedha zote hizi zipelekwe kwenye michezo. Huwezi kuwa na kitu kinachozalisha bilioni 146na hadi Juni watafika hawa bilioni 170 halafu ukawape bilioni 35 ni mzaha. Hata Rais ndoto zake hazitaweza kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine. Sports betting inategemea sana mpira wa miguu sana. Hapa Tanzania 90% ya wanaocheza betting wana bet katika michezo ya mpira wa miguu hivyo industry ile inafaidika na mpira wa miguu. Tunarudisha nini na kwa hali hii nilikuwa nashauri Serikali ichukueni hili suala kwamba iwe ni sharti la kikanuni ya kupata leseni kwamba Kampuni ya Betting ili ipate leseni ilazimike kudhamini premier league clubs ama championship club hapo tutakwenda kusaidia nchi yetu katika michezo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hili hatuna budi kupongeza zile kampuni ambazo zimejitokeza sasa hivi, kuweza kudhamini clubs zetu mbalimbali naomba nizitaje chache tu. M-Bet wanaidhamini club moja iko hapa Msimbazi inaitwa nini? Simba, kuna kampuni inaitwa Meridian wanadhamini timu ya KMC, kuna Kampuni ya Ten Bet inadhamini Dodoma Jiji. Lakini bingwa wao Sports Pesa wanadhamini Young Africans, wanadhamini Namungo, wanadhamini Singida Big Stars. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tarimba.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, sawa lakini Wizara toeni recognition kwa hawa watu ambao wanafanya vizuri ku-sponsor michezo yetu nchini. Naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kutoa mchango wangu katika hali ya uchumi wa Taifa na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa mwaka wa fedha ujao, 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba kabisa moja kwa moja niseme naunga mkono hoja hii, na wala sitasubiri mpaka mwisho wa mazungumzo yangu, nataka niseme mapema. Ninatamka hivi kwa sababu kule Kinondoni, na ndugu zangu wa Kinondoni na wananchi wa Kinondoni, tunaiona bajeti hii kwamba ni bajeti ambayo ina maono na matarajio ya wana Kinondoni, kwa hali kubwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hiyo, nataka nimpongeze kwanza Mheshimiwa Rais. Na mimi sichoki kumpongeza kwa sababu haya ambayo nitakwenda kuyazungumza yanaakisi pongezi zangu kwa nini nampongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze mwananchi mwenzangu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, na msaidizi wake, Mheshimiwa Hamad, hawa watu wanafanya kazi vizuri. Nawapenda kwa sababu wako creative, wanatuletea mambo ambayo yanamgusa Mtanzania wa kawaida kila siku. Na haya ndiyo maono ya Mheshimiwa Rais, mnayatekeleza kwa vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa nini nasema nataka Watanzania maana yake leo nazungumza na Taifa hili nikitoka Bungeni, Watanzania wanisikie huko. Kwamba pale Kinondoni kuna Kata inaitwa Kinondoni, ndiyo kata ambayo inachukua jina la jimbo, lakini jina la Wilaya ya Kinondoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kata ile kwa miaka yote hii tangu tupate Uhuru haijawahi kuwa na secondary school. You can imagine. Yaani hebu fikiria kata iko mjini lakini secondary school ya Serikali haikuwa nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimshukuru Mheshimiwa Rais, mwaka 2021 tukaja na ujumbe wetu hapa kuwaona Mawaziri wa TAMISEMI kuwaeleza matatizo tuliyonayo pale Kinondoni, wakatupatia shilingi milioni 600. Tunajenga shule ambayo ni afadhali imechelewa lakini ni shule ya kisasa. Ahsante sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hilo tu; hatukuwa hata na zahanati au kituo cha afya pale katika kata kubwa kama ile. Leo hivi tuna kituo cha afya cha kisasa kasoro tu mtutafutie madaktari wa kutosha na wauguzi, ili kisionekane kinapwaya, kitimie kabisa kile kituo cha kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nataka niipongeze Serikali, ingawa hapa kuna tatizo kidogo fedha ambazo Serikali imetupatia nilivyokuja kuomba fedha hapa milioni 600 zikapelekwa Dar es Salaam kwa ajili ya shule ya Sekondari ya Tandale. Mwaka 2021, Mheshimiwa Waziri na Mawaziri miliopo hapa, fedha zile hazikujenga secondary school.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tandale ni mahali ambapo pana idadi kubwa sana ya wananchi, na hata mahitaji ya elimu kwa watoto wanaokaa pale, watoto maskini. Serikali ilifanya kitu wanaita household budget survey kuangalia hali ya umaskini inaletwa na nini. Kaya ambazo hazina watu ambao wamekwenda shule, wamepata elimu ili iwasaidie katika maisha yao huwa wanatengeneza umaskini, hasa katika maeneo ya mjini, kwa mujibu wa bajeti hii inavyoeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kule tumepeleka hela kwa ajili ya kujenga secondary school, secondary school haijajengwa. Natamani Serikali ichunguze sababu zilizofanya secondary school ile isijengwe na fedha zile zikapelekwa kwenye jimbo lingine. Hili jambo linanichukiza sana, linatia doa kazi nzuri ya mama Dkt. Samia Suluhu Hassan.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali ifanyie utafiti kwa nini secondary school Tandale, mahali ambapo pana primary schools tatu bado wanashindwa kuweza kupata secondary school.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niipongeze Serikali kwa kumalizia Mto Ng’ombe. Sasa hivi maeneo yale ya Magomeni, Ndugumbi na Makumbusho mafuriko hayapo, mmetusaidia sana kuokoa maisha ya wananchi pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo tunalisubiri kwa hamu ni ujenzi wa Mto Msimbazi pamoja na Daraja la Magomeni. Hivyo watu wa Kinondoni wamekaa mkao wa kula wanasubiri hayo mambo. Nataka Mheshimiwa Waziri aje tu awatoe wasiwasi kwamba mradi wa Mto Msimbazi unaendelea kama ulivyopangwa. Ninajua sasa hivi watu wanalipwa fidia, kwa wale ambao watapisha mradi ule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka niipongeze tena Serikali kwa kazi nzuri wanayoifanya ya kukusanya mapato. Serikali imeonesha kwamba ukiangalia uwiano wa kodi na Pato la Taifa imejitahidi imefikia asilimia 12.5, hongereni sana. Lakini ningependa nione kwamba Serikali yangu inakusanya angalau asilimia 15 ya Pato la Taifa kama kodi kwa sababu huo ndio uwiano ambao utatusaidia kuondokana na bajeti deficit.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna nchi kama Lesotho wanakusanya asilimia 30.8 ya Pato la Taifa, nchi kama Namibia asilimia 28.27, Zambia wanafanya vizuri asilimia 16. Ninapenda nione tunaweza tukajifunza mambo gani kutoka kwenye nchi hizi ili tuweze kukusanya mapato ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo moja ambalo nilikuwa nikiliangalia halinipi furaha, nalo linahusiana na matumizi ya EFD. EFD inatusaidia sana kukusanya VAT, EFD ndiyo iko kwenye story ya kwenda kununua bidhaa ukinunua unaambiwa una risiti…ohoo!

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Hitimisha Mheshimiwa.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba niiambie Serikali ifanye utaratibu wa kutumia mifumo. Elimu ya dai risiti toa risiti haitusaidii. Tangu VAT imeanzishwa mwaka 2010 mpaka leo miaka kumi na tatu bado tunaimba wimbo huo huo na watu hawatoi risiti. Sasa ningeomba mtumie mifumo ya stock verification na stock controls ili kuweza kuondokana na shida hii ya utoaji wa risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nichangie katika hotuba hii ya Wizara ya Fedha. Mimi nitakuwa na michango miwili tu kama muda utaniruhusu nitazungumzia ufanisi uliopo katika Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa maana ya TRA na baadaye nitagusia haja ya kupanua wigo wa kodi na vilevile kuitaka Serikali au kuiomba Serikali iangalie tena nafasi yake katika utekelezaji wa blue print kwa madhumuni ya kuweza kuchagiza ufanyaji wa biashara katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, hakuna mtu ambaye anabisha kwamba Serikali inahitaji kukusanya mapato, hakuna mtu anayebisha katika hilo; na ili tuweze kufanikisha maisha bora ya Watanzania lazima Serikali iweze kufanikiwa na ndiyo kazi yetu sisi kuweza kuishauri Serikali iweze ikafanya vizuri na hata ukiangalia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri numbers ambazo amezionesha kutokana na performance ya ukusanyaji wa mapato ya Serikali katika kipindi hadi kufikia Aprili inaonesha kwamba wamefanya vizuri. Kwa sababu ni average ya asilimia 90 na kwenda juu, hivyo kama ni Chuo Kikuu Mheshimiwa Mwigulu umefanya performance ya “A” ama A plus na hapa lazima nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa sababu Mheshimiwa Rais ndiyo captain wa timu hii ya kina Mwigulu. Nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri kwa sababu naamini hata uwekaji watu sahihi katika maeneo sahihi ya Wizara ya Fedha na TRA yameweza kutuletea mafanikio haya ambayo tunayazungumza leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nilikuwa naangalia andiko la ActionAid ambalo andiko hili limetolewa mwaka 2021 wenyewe wameliita Sealing the Gaps. Walikuwa wanaangalia mfumo wetu wa kikodi na kimapato, wakaona kwamba kuna matundu ambayo yanasababisha nchi yetu tusiweze tukafikia ukusanyaji bora wa mapato na wenyewe wanakisia kwamba kuna shilingi trilioni 17.4 yawezekana zinaeleaelea na Serikali hazikusanyi ni fedha nyingi sana. Na wenyewe wanasema kuna changamoto za usimamiaji wa masuala ya kodi, wanasema kuna kodi ambazo hazilipwi na hazikusanywi, watu wachache kwa maana ya wigo ni mdogo mno wa watu ambao wanaotozwa kodi na kwa hali hii wanashabikia utanuzi wa wigo wa ulipaji wa kodi, haya ni maneno mazuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na ukiaangalia sisi tunayafahamu naamini hata Serikali inafahamu na kwa kuwa Serikali inafahamu, ni dhahiri kinachofanyika sasa kwa performance hii naweza nikasema tayari tumeanza kuona njia sahihi ya kuweza kwenda.

Mheshimiwa Spika, lakini ukiiangalia TRA hii hakika inafanya kazi nzuri ingawa ina challenges kubwa sana, ina changamoto nyingi, kwa mfano miaka mingi TRA imekuwa ikipiga kelele kuhusu kuongezewa idadi ya wafanyakazi. Na ni mpaka juzi walikuwa na watu 4,000 na ushee. Nashukuru Serikali kwamba wamewaongezea ajira ya watu 2,000 kama tulivyosikia katika hotuba hapa, lakini hitaji lao sasa hivi ni watu 8,000 na ushee maana yake kwamba bado kuna deficit, kuna upungufu wa watu 2,000.

Sasa kutokana na upungufu huo na ukiongezea ukweli kwamba mifumo ambayo ingeweza ku-support masuala mazima ya administration ya kodi hakika TRA wangeweza kufanya vizuri zaidi. Nataka niwape mfano mmoja mdogo tu, katika Bunge lako hili niliwahi kusimama na kuzungumza kuhusu kuongeza au kuweka Maafisa Kodi kwenye kila kata na nikatoa mfano, kama tuna Maafisa Ugani, kama kuna Maafisa wa Ustawi wa Jamii kwa nini tusiwe na Maafisa Kodi kwenye kila Kata. Nashukuru na naipongeza TRA walisikia ushauri ule na hata kwenye Kamati yetu tukatoa tena ushauri ule. Walichofanya ni nini, walikusanya vijana 250 kule Dar es Salaam wakawapeleka katika maeneo ya Kinondoni, Ilala, Tegeta na Temeke ili kwenda kuangalia ufanyaji wa biashara na kuweza kuangalia kama kila anayefanya biashara anatambuliwa na amesajiliwa kwa maana ya mlipa kodi.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwezi mmoja ama miezi miwili waligundua wafanyabiashara 27,463 hawakuwemo katika mfumo wa kodi. Sasa hiyo maana yake ni kwamba katika kipindi kirefu kuna watu ambao wanafanya biashara, lakini hawalipi kodi stahiki. Hivyo mimi niwapongeze TRA na niipongeze Serikali kwamba kumbe mnaweza mkatusikiliza Wabunge na mkayachukua yale ambayo tunawashauri na mkafanyia kazi, hongereni sana kwa hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nisemee kuhusu mifumo, yawezekana tukawa na watu mahiri, skilled katika maeneo mengi TRA, lakini bila ya kuwa na mifumo imara hawawezi wakafanikiwa. Hebu angalia kwa mwezi Machi ambapo mfumo wa e-filing wa VAT Returns zile za kulipia VAT walianzisha mfumo wao mwezi wa tatu na ukiongeza idadi ya wafanyakazi ambao wamewapata performance imekuwa ni nzuri sana. Performance yao ukiiangalia kwa mwezi Machi kodi za ndani zilifikia asilimia 111.5 hongereni sana TRA kwa kazi hiyo. (Makofi)

Lakini vilevile ukiangalia upande wa VAT mwezi Aprili walifikia asilimia 103.8 performance yao kuzidi malengo na ukiangaliza namba zote wame exceed malengo waliyojiwekea. Maana yake ni kwamba endapo watakuwa na mifumo sahihi kama ilivyo hii ya VAT ni dhahiri kabisa Serikali inaweza ikafanya vizuri na hapa nataka niikumbushe Serikali kuna mfumo mmoja unaitwa IDRAS nilikuwa nateta na mwananchi mwenzangu pale bigwa Mheshimiwa Mwigulu kwamba IDRAS ni mfumo ambao utaisaidia sana Serikali katika kupata fedha kupitia kodi za ndani.

Mheshimiwa Spika, hiyo ni kengele ya kwangu hiyo?

SPIKA: Hapana.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Sawa ahsante.

Mheshimiwa Spika, IDRAS ndiyo mwarobaini kwa sababu IDRAS itasimamia vizuri sana mifumo ya kodi za ndani kama ilivyo katika VAT kiasi kwamba mfumo huu ukiwa mahiri utaweza kuzungumza na mifumo mingine. Serikali imeonesha utayari wenu, sasa huu mfumo tunajua ni ghali na ilikuwepo na juhudi kuupata tangu Serikali ya Awamu ya Tano, lakini ile tender ika-fail. Sasa msitafute wafadhili, Mheshimiwa Waziri msitafute wafadhili, Serikali igharamie yenyewe mfumo huu, huu mfumo ndiyo utatuondolea matatizo. Angalia mfumo huu unaweza ukajumuishwa na miamala ya simu, mfumo huu unaweza ukajumuishwa na Forodha...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Sekunde 30 malizia sentensi.

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, mifumo ya Forodha na mifumo mingine yote ya NSSF. Kiasi kwamba hata component ya pay as you earn mtaipata ya kutosha kuliko ilivyo hivi sasa.

Mheshimiwa Spika, hivyo ningeiomba Serikali inapokuja kumalizia na kutoa hitimisho itueleze inajipanga vipi kuhakikisha kodi za ndani zinapata mfumo mahiri ili kuweza kutusaidia kukusanya fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja hii. Ahsante sana. (Makofi)
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) (no. 6) Bill, 2021
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia katika Muswada ulioletwa na Serikali unaohusiana na mabadiliko ya Sheria Mbalimbali Namba (6), 2021 ambao umeletwa kwa ajili ya Wabunge tuweze kuubariki na kuwa sheria. Jambo la kwanza ningependa nichangie kwenye upande wa kile Kifungu 83(b) ambacho ni cha Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura 332.

Mheshimiwa Spika, ningeanza kusema yafuatayo. Kwanza jambo hili lilitaka lituponze Kamati ya Bajeti, laiti kama Serikali ingekuwa inaendeleza ule utulivu wake na usikivu wake wanapokutana na Kamati ya Bajeti yawezekana hata lile tatizo la kuweza kukusanya fedha hizi kuanzia mwezi wa Julai, kama Mheshimiwa Vita alivyokuwa anazungumza, lingeweza kuepukika. Ninakimbilia niseme kwamba, katika siku zijazo Serikali inavyokutana kupata ushauri na Kamati ya Bajeti ningeomba sana wachukue ushauri ule na kuufanyia kazi, kwa sababu leo hii kuna watu waliumia kuanzia mwezi wa saba.

Mheshimiwa Spika, uelewe kilimo kinaajiri zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania na hasa ukiondoa pengine asilimia tano ya wakulima wakubwa, waliobakia ni wakulima wa kawaida wadogowadogo ambao wengi sana ni hand to mouth. Sasa hii sheria ilivyokuwa imefanya kazi hakika iliwaumiza watu na bahati mbaya sana sheria haiwezi ikawa retrospective, lakini ningetamani kama ingekuwa inawezekana ikarudi nyuma kuweza kuwaokoa wale ambao waliweza kuchangia pasi na kuweza kujua kwamba sheria hii hakika ina kero kubwa.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi naipongeza Serikali. Naipongeza kwa dhati kabisa Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kuja na mapendekezo haya ambayo sasa mimi naona kama hatujachelewa ingawa wapo walioumia, lakini ninaamini mara baada ya Bunge lako Tukufu litakapopitisha mabadiliko haya Rais nae hatachelewa kuisaini ili sheria hii iweze kuanza kutumika mapema sana.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; Leo hii kwa marekebisho ya Sura ya 438, ile Sheria ya Usimamizi wa Kodi ambayo tunakwenda kuirekebisha sasa hivi inakamilisha hatma ya Serikali katika kuhakikisha zile reliefs ambazo zinahitajika kutokana na mkataba wa kati ya Tanzania na Uganda juu ya utengenezaji wa hili bomba la mafuta leo hii taratibu zile zinakwenda kukamilika. Kwa sababu tulishapitisha na kufanya marekebisho ya sheria nyingi sana, ilibakia a fiscal reliefs na leo inakwenda kukamilika na mimi naweza nikasema ninaunga mkono na ninaomba Waheshimiwa Wabunge wa Bunge lako la Tanzania liweze kukubali mabadiliko haya ambayo yamefanywa na Serikali ili sasa mradi huu muhimu ambao tumekuwa tukiusubiri na tuliokuwa tukiugombania sana Tanzania na nchi nyingine uweze kwenda ukafanye kazi.

Mheshimiwa Spika, mwisho kama utaniruhusu, Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti alilizungumzia suala la tax ombudsman jambo hili linaleta ukakasi mkubwa sana kwa upande wa Serikali. Inawezekana isiwe ni subject matter ya majadiliano ya sasa hivi, lakini lina umuhimu kwa Taifa letu kwamba, kule katika tax tribunal kuna kesi nyingi yenye thamani ya zaidi ya trilioni 2.6 yamekwama. Ni nini ukakasi wa Serikali kuanzisha tax ombudsman ambapo ni sheria iliyoishapitishwa na Bunge lako Tukufu miaka mitatu imeshapita. Ni king’ang’anizi gani na uwoga gani wa kuanzisha hicho kitu?

Mheshimiwa Spika, Serikali tunachohitaji sisi ni mapato kwa ajili ya Taifa letu ili yaweze kwenda kusaidia shughuli nyingine nyingi sana. Trilioni 2.6 ni hela nyingi, hata kama tukizipata nusu kwa usuluhishi chini ya ofisi ya msuluhishi tax ombudsman yawezekana tukapiga hatua sana. Naiomba Serikali wakati itakapokuja kufanya winding up ya Muswada huu waweze kutugusia ni kitu gani kinachowafanya wakachelewa kiasi hiki kuweza kuanzisha ofisi hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie muswada ambao uko mbele yetu. Kwa haraka kabisa niweze kuipongeza Serikali kwa kuleta Muswada huu na vilevile niwapongeze Mheshimiwa Waziri, mwananchi Mwigulu pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Chande pamoja na Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambao tumeshinda nao kwa kipindi cha siku mbili kuweza kushauriana jinsi ya kuuboresha Muswada huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania ni sehemu ya jumuiya ya kimataifa. Matukio ya utakatishaji wa fedha popote pale yanapotokea na hasa vile vile yakitokea hapa nyumbani yanatuathiri vibaya mno katika miundombinu, katika masuala ya kuweka usalama wa nchi yetu na hata masuala yanayohusu uchumi wetu kwa ujumla. Hivyo ni vitendo ambavyo vinaweza vikasababisha kutokuwepo na amani, maendeleo na hata ikapelekea kutengwa na mashirika ya kimataifa na nchi nyingine ambazo zinatuona Tanzania kama vile hatuna sheria madhubuti za kupambana na utakatishaji wa fedha pamoja na ufadhili wa fedha haramu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hii, kama ilivyosemwa na Mheshimiwa Waziri Mwenyekiti pamoja na maoni ya Kamati, kwamba Tanzania inaonekana kana kwamba tuna viashiria vya kati na vya juu vinavyohusiana na masuala ya utakatishwaji wa fedha. Hivyo ningeomba Bunge hili liridhie na kukubali mabadiliko haya ya sheria ili sasa tuweze kukumbana na kupambana vilivyo na matukio haya ya utakatishaji wa fedha na financing of terrorism.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu ambacho kimenifurahisha. Katika tafsiri ya sheria ambayo kwanza ililetwa, inayohusiana na maana ya familia, wakawaongeza wazazi na wakwe. Katika tasnia ya Kiafrika kumtaja mzazi katika masuala kama haya na vilevile wakwe inatuletea ukakasi. Nimefurahi kuona kwamba Serikali imekubaliana na Kamati kutumia tafsiri ya financial action task force ile ya kimataifa kwa kuwaondoa watu hawa wasiwemo katika tafsiri ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, hii haimaanishi kwamba yule ambaye ataonekana kufanya vitendo vya kutakatisha fedha na akazipenyeza na kuzichepusha kwa wazazi au wakwe sheria haitamuacha, hiyo imenifurahisha, ingawa hawakumtaja jina lakini tusitumie mwanya huo kuwapelekea wazazi wetu fedha ambazo ni chafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na suala linalohusiana na masuala ya due diligence, ningeomba na kuikumbusha Serikali iharakishe kuja na guidelines za jinsi taasisi za kifedha zinavyotakiwa zifanye hiyo exercise ya due diligence.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia zaidi Muswada huu utaongeza majukumu ya FIU kutoka majukumu tisa hadi 15. Napata mashaka juu ya utekelezaji wa sheria hii. Nikiwaangalia capacity ya FIU, workforce ya FIU, nikiangalia ufundi wa masuala ambayo yamezungumzwa, nikiangalia na bajeti, ambapo mwaka huu wamewekewa 1.29 billion shillings naona kana kwamba sheria hii inaweza ikafika mahali isiweze kutekelezwa vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na hilo, naiomba Serikali, na ningependa mwananchi wakati atakapokuja kufanya hitimisho atueleze ni kwa jinsi gani Serikali inajipanga kuweza kuifanya FIU iwe na bajeti ya kutosha, iwe na wafanyakazi wa kutosha, lakini vile vile ifikirie pia kuipandisha hadhi FIU isibaki kama unit bali iendelee na kupata hadhi ya juu ili iweze kutekeleza matakwa haya ya kisheria vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata pale tutakapofanyia peer review iweze ikaonekana kwamba kweli Tanzania wamefanya marekebisho ya sheria hizi ili kuweza kukidhi na kufikia viwango vya Kimataifa. Pale ninavyotaja mwananchi, maana yake nazungumzia Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, mwananchi ambaye kwenye hili ni bingwa kabisa. Ninaamini haya ambayo tumependekeza, kama ilivyokuwa katika Kamati kuyapokea maoni ya Kamati, basi hata hapa maoni ya Wabunge ataweza kuyapokea vizuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hali hiyo, naunga mkono hoja. Ahsante sana kwa kunipa nafasi. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa dhati kabisa kwa kunipa nafasi hii, Mungu akubariki sana kwa kazi nzuri ambayo unaifanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitajielekeza katika hoja iliyoko mbele yetu, Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022. Kabla sijaendelea na mchango wangu, naomba niunge mkono hoja hii na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge waweze moja kwa moja kuupitisha huu Muswada na kuwa sheria.

Mheshimiwa Spika, nazungumza kwanza katika mtazamo wa mwekezaji. Mimi Alhamdulillah nashukuru pia ni mmoja kati ya wawekezaji. Wawekezaji wana mitazamo yao, Serikali ina mitazamo yake. Sasa hebu tuangalie mtazamo wa mwekezaji. Mtazamo wa mwekezaji uko katika sura mbili sana, wamekubaliana ni sura mbili. Sura ya kwanza wanajiuliza: Je, hii fedha yangu ninapoipeleka itafanya kazi ya kuleta faida? Ndiyo kitu kikubwa. Pale wanaangalia kitu wanakiita the power of compounding; Kiswahili chake kidogo kinanipa mashaka. Upande mwingine wanaangalia risk na returns katika investments.

Mheshimiwa Spika, sasa hebu tuangalie the power of compounding. Hapa wanasema ni utaratibu wa uwekezaji ambao unakuhakikishia kupata faida na gawio ambalo pengine unaweza ukalitumia kuendeleza biashara yako ile ile ama kutengeneza investment nyingine. Hao ndio investors.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali, wao wanaangalia sababu tatu kuu, kwa nini kuwepo na investment? La kwanza, wanaangalia mapato ya Serikali kwa maana ya kodi, ile investment itengeneze utaratibu wa kuipatia Serikali mapato. Vilevile uwekezaji usaidie kuboresha hali ya kifedha kwa watu pale wanapofanya shughuli za kibiashara katika zile investments ambazo zimewekwa. Ya tatu, kuleta ajira na mambo mengine ambayo yanahusiana.

Mheshimiwa Spika, sasa ukiangalia katika jambo kama hilo, kuja na Muswada kama huu maana yake sasa tunajielekeza katika ule utaratibu ambao tunajiuliza kumbe ni muhimu sana kwa Serikali kuleta utaratibu mzuri wa uwekezaji katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri zaidi kuliangalia lile ambalo Waheshimiwa Wabunge wengine wamelizungumzia; ease of doing business. Tuipongeze Serikali kwa juhudi kubwa ambazo wameanza kuzifanya katika mwaka wa fedha huu tulionao wakati tukipitisha bajeti. Sheria karibu 14 na zaidi zimeangaliwa na kufanyiwa marekebisho. Nini faida yake? Hebu tuangalie faida ya yale madogo tu tuliyoyafanya katika masuala mazima ya ease of doing business.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungimzia hapa position yetu tuliyokuwanayo. Mwaka 2019 tulikuwa ni nchi ya 141 kutoka kwenye nafasi ya 144 mwaka 2018. Sasa wataalam wa World Bank wanasema mwaka 2022, huu tulionao, yawezekana tukapanda tukawa ni nchi ya 138 kwenye vile vigezo vyao. Mwaka 2024 outlook inaonesha tutapanda kufikia nchi ya 136, maana yake Tanzania tunapiga hatua.

Mheshimiwa Spika, kama tunapiga hatua, lakini hatua zenyewe ni ndogo, siyo kubwa, naishauri Serikali kwamba kwa kuwa yawezekana kupiga hatua kwa kufanya marekebisho katika sheria zetu, na siyo tu sheria ya uwekezaji, tuangalie supporting laws nyingine, kwa sababu sheria ya uwekezaji ni sheria mama, lakini kuna sheria nyingine zinazotusaidia kwa mfano, sheria za kodi, sheria za upatikanaji wa business licenses, sheria za repatriation ya faida na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kuna haja sasa kwa Serikali kuangalia katika nchi zikiwemo nchi ambazo ziko karibu, ameizunguumzia sana Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla; maeneo ambayo yamefanya vizuri na siyo tu kutegemea kufanya mambo ya kubahatisha. I am sorry natumia neno “kubahatisha”, kwa maana pengine hii itafanya kazi ama haitafanya kazi, lakini cha msingi ni kutafuta yale maeneo ya kisheria ama ya kiuendeshaji ambayo tukiyafanyia marekebisho, hakika yatatupa quick wins. Tuna kazi ya kufanya na lazima tuziangalie hizo taratibu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuangalia yote hayo, kuna juhudi hapa zinafanywa na Mheshimiwa Rais. Nataka nilete mfano wa juhudi aliyoifanya alipokwenda Dubai Expo mwaka 2021. Kulikuwa na MOUs nyingi sana pale zimesainiwa, kuna mikataba mingi pale imesainiwa; nilitaka nijue baada ya kusainiwa yale mambo ambayo yanavutia investment kwa Tanzania, ni vipi sasa Serikali imejikita katika kuhakikisha kwamba mambo yale yanaendelezwa na kweli yanatuletea tija katika uwekezaji wa nchi yetu?

Mheshimiwa Spika, tunaboresha sheria, naam, lakini sheria peke yake bila ya sisi kubadilika na kuwa ni watu ambao tunaendana na dunia ya sasa inayokaribisha investment na investors wasionekane ni maadui; kulikuwa na wakati investors hapa walikuwa wanakimbiakimbia sana, tuwakaribishe.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Tanzania huko nje, sisi ambao tunapata nafasi ya kuzungumza na wenzetu, tunaona wanaiangalia Tanzania kama moja ya nchi ambayo imefanya marekebisho makubwa sana katika sheria zake za kukaribbisha investment. Hivyo, tuchukue mtazamo huo ambao ni mzuri kufanya Tanzania ineemeke na Mtanzania mmoja mmoja aneemeke kwenye njia kama hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, na kwa ushauri huo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Mwaka 2022
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa dhati kabisa kwa kunipa nafasi hii, Mungu akubariki sana kwa kazi nzuri ambayo unaifanya.

Mheshimiwa Spika, mimi nitajielekeza katika hoja iliyoko mbele yetu, Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022. Kabla sijaendelea na mchango wangu, naomba niunge mkono hoja hii na kuwaomba Waheshimiwa Wabunge waweze moja kwa moja kuupitisha huu Muswada na kuwa sheria.

Mheshimiwa Spika, nazungumza kwanza katika mtazamo wa mwekezaji. Mimi Alhamdulillah nashukuru pia ni mmoja kati ya wawekezaji. Wawekezaji wana mitazamo yao, Serikali ina mitazamo yake. Sasa hebu tuangalie mtazamo wa mwekezaji. Mtazamo wa mwekezaji uko katika sura mbili sana, wamekubaliana ni sura mbili. Sura ya kwanza wanajiuliza: Je, hii fedha yangu ninapoipeleka itafanya kazi ya kuleta faida? Ndiyo kitu kikubwa. Pale wanaangalia kitu wanakiita the power of compounding; Kiswahili chake kidogo kinanipa mashaka. Upande mwingine wanaangalia risk na returns katika investments.

Mheshimiwa Spika, sasa hebu tuangalie the power of compounding. Hapa wanasema ni utaratibu wa uwekezaji ambao unakuhakikishia kupata faida na gawio ambalo pengine unaweza ukalitumia kuendeleza biashara yako ile ile ama kutengeneza investment nyingine. Hao ndio investors.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali, wao wanaangalia sababu tatu kuu, kwa nini kuwepo na investment? La kwanza, wanaangalia mapato ya Serikali kwa maana ya kodi, ile investment itengeneze utaratibu wa kuipatia Serikali mapato. Vilevile uwekezaji usaidie kuboresha hali ya kifedha kwa watu pale wanapofanya shughuli za kibiashara katika zile investments ambazo zimewekwa. Ya tatu, kuleta ajira na mambo mengine ambayo yanahusiana.

Mheshimiwa Spika, sasa ukiangalia katika jambo kama hilo, kuja na Muswada kama huu maana yake sasa tunajielekeza katika ule utaratibu ambao tunajiuliza kumbe ni muhimu sana kwa Serikali kuleta utaratibu mzuri wa uwekezaji katika nchi hii.

Mheshimiwa Spika, ni vizuri zaidi kuliangalia lile ambalo Waheshimiwa Wabunge wengine wamelizungumzia; ease of doing business. Tuipongeze Serikali kwa juhudi kubwa ambazo wameanza kuzifanya katika mwaka wa fedha huu tulionao wakati tukipitisha bajeti. Sheria karibu 14 na zaidi zimeangaliwa na kufanyiwa marekebisho. Nini faida yake? Hebu tuangalie faida ya yale madogo tu tuliyoyafanya katika masuala mazima ya ease of doing business.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge wamezungimzia hapa position yetu tuliyokuwanayo. Mwaka 2019 tulikuwa ni nchi ya 141 kutoka kwenye nafasi ya 144 mwaka 2018. Sasa wataalam wa World Bank wanasema mwaka 2022, huu tulionao, yawezekana tukapanda tukawa ni nchi ya 138 kwenye vile vigezo vyao. Mwaka 2024 outlook inaonesha tutapanda kufikia nchi ya 136, maana yake Tanzania tunapiga hatua.

Mheshimiwa Spika, kama tunapiga hatua, lakini hatua zenyewe ni ndogo, siyo kubwa, naishauri Serikali kwamba kwa kuwa yawezekana kupiga hatua kwa kufanya marekebisho katika sheria zetu, na siyo tu sheria ya uwekezaji, tuangalie supporting laws nyingine, kwa sababu sheria ya uwekezaji ni sheria mama, lakini kuna sheria nyingine zinazotusaidia kwa mfano, sheria za kodi, sheria za upatikanaji wa business licenses, sheria za repatriation ya faida na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, kuna haja sasa kwa Serikali kuangalia katika nchi zikiwemo nchi ambazo ziko karibu, ameizunguumzia sana Mheshimiwa Dkt. Kigwangalla; maeneo ambayo yamefanya vizuri na siyo tu kutegemea kufanya mambo ya kubahatisha. I am sorry natumia neno “kubahatisha”, kwa maana pengine hii itafanya kazi ama haitafanya kazi, lakini cha msingi ni kutafuta yale maeneo ya kisheria ama ya kiuendeshaji ambayo tukiyafanyia marekebisho, hakika yatatupa quick wins. Tuna kazi ya kufanya na lazima tuziangalie hizo taratibu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuangalia yote hayo, kuna juhudi hapa zinafanywa na Mheshimiwa Rais. Nataka nilete mfano wa juhudi aliyoifanya alipokwenda Dubai Expo mwaka 2021. Kulikuwa na MOUs nyingi sana pale zimesainiwa, kuna mikataba mingi pale imesainiwa; nilitaka nijue baada ya kusainiwa yale mambo ambayo yanavutia investment kwa Tanzania, ni vipi sasa Serikali imejikita katika kuhakikisha kwamba mambo yale yanaendelezwa na kweli yanatuletea tija katika uwekezaji wa nchi yetu?

Mheshimiwa Spika, tunaboresha sheria, naam, lakini sheria peke yake bila ya sisi kubadilika na kuwa ni watu ambao tunaendana na dunia ya sasa inayokaribisha investment na investors wasionekane ni maadui; kulikuwa na wakati investors hapa walikuwa wanakimbiakimbia sana, tuwakaribishe.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Tanzania huko nje, sisi ambao tunapata nafasi ya kuzungumza na wenzetu, tunaona wanaiangalia Tanzania kama moja ya nchi ambayo imefanya marekebisho makubwa sana katika sheria zake za kukaribbisha investment. Hivyo, tuchukue mtazamo huo ambao ni mzuri kufanya Tanzania ineemeke na Mtanzania mmoja mmoja aneemeke kwenye njia kama hii.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, na kwa ushauri huo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)