Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Salim Alaudin Hasham (7 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bunge lako Tukufu japo ametumia jina langu Salimu Almas jina la biashara jina langu kamili naitwa Salimu Alaudin Hasham Mbunge wa Jimbo la Ulanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niniiponge Wizara kwa kazi kubwa waliofanya kwa kuleta mabadiliko makubwa katika sekta ya madini mpaka hii leo kuonekana sisi pia wachimbaji wadogo ni watu ambao tunachangia katika pato la Taifa. Lakini kuna vitu vichache ambavyo napenda kuvichangia kwenye Wizara ya Madini ili kuviweka sawa inawezekana ikachangia pato zaidi kwenye upande wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natokea kwenye upande wa madini ya vito na nimekulia kwenye madini ya vito cha kwanza kabisa naomba nichangie katika upande wa value addition. Kwenye upande wa value addition, Tanzania tuna madini ya aina nyingi sana na Tanzania inaachangia duniani kwa asilimia karibu 30 kwenye madini ambayo yanaingia kwenye soko la dunia.

Lakini niseme ukweli kabisa kwamba Serikali bado hatujajipanga vizuri kwenye upande wa value addition na hii nitatoa mifano michache kutokana na ufinyu wa muda mfano mkubwa kabisa tuna madini aina ya safaya ambazo zinachimbwa Tanga na ambayo yanachimbwa Tunduru kwenye Jimbo la ndugu yangu Hassani. (Makofi)

Mheshimimiwa Naibu Spika, madini yale yamewekwa kwenye utaratibu kwamba mwongozo unasema madini yale yasafirishwe kuanzia gramu mbili kushuka chini ndio yasafirishwe yakiwa ghafi. Kwa maana hiyo kwamba madini ya juu hayawezi kusafishwa lakini kinachotokea ni kwamba kwenye upande wa safaya madini ya safaya ili yaweze kuongeza thamani lazima yafanyiwe treatment kwa maana yachomwe na utaalamu ule bado haujaingia kwenye nchi yetu kabisa huko Thailand peke yake na hawajawahi kuugawa utaalamu ule kwenye nchi zingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo Serikali itakuwa imeamua kuuwa biashara ya madini aina ya safaya, vinginevyo wangeruhusu yale madini mengine yaweze kusafirishwa madini ya vito yasafirishwe yakiwa ghafi ina maana labda kuna uwezekano ingesaidia utoroshaji wa madini katika sekta ya madini. Ninayo mifano mingi lakini kutokana na ufinyu wa muda kwa sababu nina vitu vingi vya kuchangia naomba niendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna upande wa ma-valuer kiukweli Serikali ina ma-valuer wachache sana kwa upande wa Tanzania katika idadi ambayo tulionayo katika takwimu inaonyesha tuna ma-valuer 18 peke yake ambao hawatoshi lakini naamini kabisa Serikali inapambana kuongeza ma-valuer lakini pia ma-valuer wetu wengi awana uzoefu mkubwa wa kufanya valuation ya madini tuliyo nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naamini kipindi ambacho wanaendelea kufanya kazi watapata uzoefu ili kujihakikishia kazi ambayo wanaifanya. Lakini pia kuna maneno yanasemekana kwamba ma-valuer wetu ndiko mapato yanakopotelea jibu nasema sio kweli kabisa na inawezekana ma-valuer hawa wanawapatia faida zaidi Serikali kuliko wafanyabiashara kwasababu mara nyingi Serikali kuliko wafanya biashara kwasababu mara nyingi wakikosea wanakosea kwenye kuongeza thamani ya madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kodi utakayolipa itakuwa ni kubwa zaidi naomba Serikali ijikite zaidi kuangalia madini yanapotelea wapi lakini sio mapato yanakopotelea naamini kabisa madini yakifika kwa ma-valuer Serikali haina kinachopoteza. Kwa hiyo, ijikite kwenye kuangalia madini yanatoroshwa vipi lakini si yanapotea kutokana na wanaofanya valuation.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa lingine naomba nichangie na hii itakuwa ni special case Mheshimiwa Waziri unisaidie kidogo kwenye upande wa Jimbo langu kuna kampuni mbili ambazo zinataka kuja kufanya miradi mikubwa ya madini ya kinyo yaani graphite. Kampuni zile ni Tanzagraphite na ingine inaitwa Mahenge - resource. Mwaka 2017 walifanya uthamini juu ya kuwalipa fidia wana Kijiji wa Ipango, lakini mpaka mwaka 2019 uthamini ule ulikuwa ume-expire kwa maana hiyo kampuni ya Tanzagraphite ilipaswa kuwalipa posho ya usumbufu wananchi wa Ipango kulingana na kucheleweshwa na kusitishwa shughuli zao za maendeleo na waliandikiwa barua walihimizwa kwamba wafungue akaunti ili waweze kulipwa posho hizo lakini mpaka leo hawakuweza kufanya kitu kama hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, na bado watu wale wamesitishwa kabisa kufanya shughuli za maendeleo kwa hiyo nilikuwa naomba kupata muhafaka wa kampuni ile nini kinaendelea na nipate muafaka mzuri nione jinsi gani ya kuwajibu na katika sehemu ambayo nilipata changamoto kipindi nafanya kampeni zangu Mheshimiwa Waziri, nilifika niliwakuta wananchi wale wamekaa chini badala ya kunishangilia. Matokeo yake ikabidi nibadilishe mkutano kwa kikao kama cha familia ili waweze kunielewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kuna kampuni nyingine ya Mahenge resource ambayo pia imeshafanya uthamini, tunaomba pia uhalali wa kampuni ile na uhakiki wa kampuni ile kwamba ipo tayari kuja kufanya kazi katika vijiji vyetu kwasababu isije na wenyewe wakatokea ikawa kama yenyewe ni Tanzagraphite ambako wananchi wale pia wamesitishwa zaidi ya vijiji vinne havifanyi shughuli za maendeleo.

Mheshimia Naibu Spika, naomba nizungumzie kwenye value of chain kwenye upande wa madini kuna mchimbaji, kuna broker na kuna dealer, ukiweka hawa watu ukiwakusanya pamoja lazima mmoja wapo… broker ni mtu ambaye ana mtaji mdogo mwezangu na mimi au la hana mtaji kabisa. Obvious mchimbaji yule hawezi kufanya kazi na broker akachagua kufanya kazi na dealer, kwasababu wana-cash, maana yake utakuwa umemuuwa yule broker hawezi kufanya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wale tunawalazimisha wakate leseni watu wanakadiliwa kodi ya mapato mwisho wa mwaka wanapaswa kulipwa na ndio wengi zaidi ambao wanaunganisha biashara kati ya mchimbaji na dealer. Kwa hiyo, naomba pia Serikali iliangalie hili kwa kina zaidi ione ni jinsi gani inaweza kufanya mabadiliko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nirudi kwenye upande wa GST bado haijafanya vizuri sana kwenye upande wake, ningeomba Serikali iwawezeshe sana GST waende kufanya utafiti katika madini yenye thamani kubwa kama vile kama ya aluminum, copper lithium maganize nickel graphite, silver na mengine mengi lakini pia kuna layer- ath-stone kama ruby spinel na madini mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, GST iende ikafanye utafiti mkubwa ili kuongeza wawekezaji waje kwa wingi kufanya, lakini pia Serikali iwaangalie sana wawekezaji wa ndani kwa sababu wawekezaji wa ndani sasa hivi wana uwezo mkubwa wa kufanya, na iwaangalie kwa jicho la tatu ili waweze kuwasaidia na hasa kwenye upande wa mikopo ya wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo hatuamini kabisa mabenki pamoja wanashauriwa kwa ajili ya kutukopesha lakini mabenki bado hayatuamini kwa hiyo tungeifanya biashara yetu iwe biashara ambayo inatambulika duniani na watu waaamini kile ambacho tunakifanya naamini Serikali yetu ingeweza kuongeza pato zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kupata nafasi siku ya leo ya kuchangia kwenye Bunge lako Tukufu. Pia namshukuru sana Mheshimiwa Rais pamoja na Serikali yake kwa sababu wanafanya kazi nzuri sana. Nawapongeza kwa sababu kazi zinaonekana na sisi Wabunge wote humu ndani ni mashahidi wa kazi ambazo zinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitajielekeza kwenye kuchangia kwenye Wizara ya Afya na nikiapata nafasi nitachangia kwenye Wizara nyingine. Tunaishukuru sana Serikali na tunamshukuru sana Mama Samia Suluhu Hassan kwa sababu kiukweli tumepata vituo vya afya vingi sana pamoja na zahanati za kutosha sana kwenye majimbo yote ambayo Wabunge wanayamiliki. Haipingiki kwamba kazi hizi nzuri zinafanywa na Serikali ya Awamu ya Sita lakini haina maana kwamba hakuna changamoto ambazo zinaendelea kwenye maeneo yetu hasa kwenye huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mifano kadhaa kwa sababu changamoto hizi bado zipo. Kwenye mwaka wa fedha 2023 tulipata pesa shilingi milioni 200 kwenye jimbo langu. Nakupa mifano kwa sababu kuna changamoto nimeiona kati ya MSD na Serikali yetu. Nilipata shilingi milioni 200 ziligawanywa kwenye makundi mawili. Shilingi milioni 50 ilikuwa imeenda kwenye Zahanati yangu ya Minepa lakini shilingi milioni 150 imeenda kwenye kituo cha afya kipya kabisa kwenye Tarafa yangu ya Lupilo Kata ya Iragua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2018/2019 tulipata pesa shilingi milioni 300 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye Kituo cha Afya cha Lupilo. Mpaka hivi ambavyo ninaongea, shilingi milioni 50 kwenye Zahanati ya Minepa tumepata vifaa vya shilingi 3,800,000 toka mwezi wa Tano tumewalipa MSD, lakini pia kwenye vifaa tiba, kwenye Kituo changu cha Afya cha Iragua tumepata vifaa vya shilingi milioni 25 kutoka kwenye shilingi milioni 150 tangu mwezi wa Tano. Kwenye fedha tuliyoipata tangu mwaka 2018/2019 tumepata vifaa, bado tunadai vifaa vya milioni shilingi 106 kutoka MSD. Sasa hilo ndilo ambalo nililokuwa nataka kulizungumzia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwa upana kabisa, kwanza kuna tatizo kwa sababu inaonekana pia Sheria za Manunuzi zimekiukwa kwa sababu supplier huyu anaonekana alilipwa kabla ya ku-supply vitu ambavyo sisi tunavihitaji. Muda unaenda kwa sababu limeshapita, tufunike kombe mwanaharamu apite, ameshalipwa, lakini kwa nini ha-supply? Kitu ambacho nimekiona kwa MSD, na hapa Wabunge wenzangu wapo ni mashahidi, ukizungumza na Ma-DMO wanakwambia kabisa tatizo lipo MSD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa MSD ni kazi inayofanyika kati ya Serikali na MSD. Labda Serikali ituambie kuna tatizo gani kati ya MSD na Serikali? Kwa sababu inaoneka MSD wanafanya kazi vile ambavyo wao wenyewe wanajisikia kufanya. Unalipa hela mwaka 2019, leo miaka mitano vifaa vya shilingi milioni 300 havijafika kwenye hospitali yetu. Leo hii tunataka tudumishe afya bora na huduma bora za afya kwenye maeneo yetu. Namwomba sana dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa sababu amesikia changamoto hii, naomba anisaidie niweze kupata vifaa tiba ili wananchi wake na wananchi wangu pia waweze kupata huduma ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimesimama hapa karibu mara mbili kwenye Bunge hili hili nikitoa maelezo juu ya hospitali yangu ya wilaya ilivyochakaa, ina miaka zaidi ya 60. Mnamo mwaka 2017/2018 tulipata pesa za ukarabati, shilingi milioni 400, ilishindikana kufanya ukarabati kwenye hospitali ile kwa sababu ni hospitali kongwe na ni chakavu. Matokeo yake tukalazimika kuongeza majengo kwenye hospitali ile. Hivi ninavyokwambia sasa hivi, eneo lote limejaa na hatuwezi kufanya ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali kwa sababu ni kongwe, watu walikuwa 50,000 sasa hivi wameshafika kwenye 200,000, hospitali ile haiwezi kuhudumia tena wananchi wale. Ukiacha hilo pia, kuna kaka yangu, ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Biteko, Mheshimiwa Naibu Waziri alijitahidi sana kutafuta wawekezaji kwenye jimbo langu na tumepata makampuni karibu mawili na yote yameshasainiwa mkataba. Wanaenda kuajiri wafanyakazi zaidi ya 1,000 waajiriwa rasmi, na ajira ambazo siyo rasmi ni zaidi ya 3,000 mpaka 5,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itakuwa ni aibu kubwa sana leo hii wawekezaji wale wanaenda kutafuta hospitali kwenye wilaya inayofuata au mkoani kwa sababu sisi hospitali ya wilaya hatuna. Dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu nilikuomba mara ya mwisho hapa, kama huamini haya ambayo nakwambia, twende ukajionee mwenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nimeletewa shilingi milioni 900 za ukarabati tena kwenye hospitali ile ile ambayo nimesema kwamba haikarabatiki. Tunashukuru tumepata, lakini tunawaambia kwamba changamoto yetu haikuwa hiyo. Halafu mimi niliyesimama hapa mbele ndio Mwakalishi wa Wana-Ulanga, ndio najua shida za Wana-Ulanga. Leo hii hamnisikilizi mimi, sasa sijui mtakuwa mnamsikiliza nani? Kwa hiyo, namwomba dada yangu, Mheshimiwa Ummy Mwalimu na hili nalo alichukue tusaidiane. Tuna shida ya kupata hospitali ya wilaya kwa sababu kwetu imeshakuwa ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu muda wangu bado unanitosha, naomba nichangie kwenye sekta ya kilimo. Hatuna budi kuwekeza kilimo chetu kwenye skimu za umwagiliaji. Kama tunataka tupate tija kwenye kilimo nchi hii kwa sababu asilimia 80 ya Watanzania ni wakulima, basi ni lazima tuwekeze kwenye skimu za umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwangu kuna skimu kama nne ambazo zinahitajika kwenye Jimbo langu. Kuna Skimu ya Minepa ambayo haijaisha, lengo iishe iweze kuwafikia wananchi wengi zaidi. Kuna Skimu ya Lupilo ambayo imeshafanyiwa study, kuna Skimu ya Lukana ambayo imeshafanyiwa study na kuna Skimu ya sehemu moja Kata ya Euga ilijengwa tangu nikiwa mdogo haijawahi kutumika mpaka imeharibika na sijui tatizo ni nini? Huu unaonekana kabisa ni uharibifu wa fedha za Serikali kwa sababu zilitumia fedha kujenga ile skimu lakini haikutumika kwa sababu haikuisha, leo hii tunaenda tena kuianza kuijenga upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo la pili ambalo linaendelea kwenye maeneo yetu kwenye majimbo yetu; suala la stakabadhi ghalani. Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan alivyokuwa Singida alielekeza watendaji wake kwa maana ya Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi waende wakaangalie namna sahihi ya kuliingiza zao la mbaazi kwenye kuliuza kwenye stakabadhi ghalani. Jamani haikuwa sheria, kuna baadhi ya watendaji wetu na viongozi wana tabia ya kumfurahisha Mheshimiwa Rais, hatuko hapa kwa ajili ya kumfurahisha Mheshimiwa Rais jamani. Tuko hapa kwa ajili ya kumsaidia Mheshimiwa Rais na wale ambao huwa wanafanya maamuzi ya kumfurahisha Mheshimiwa Rais mkifika wakati wa uchaguzi hawaingii uwanjani kucheza, wanatuletea shida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo wananchi hawako tayari kulifanya, halina afya kwa wananchi wala halina afya kwa sisi viongozi ambao wa kuchaguliwa katika maeneo yetu, kwa sababu ukifanya hivyo wananchi hawa kuna mwananchi analima yuko sehemu ya mbali kabisa ana debe zake mbili ghala liko kilometa 50 kutoka alipo, abebe debe mbili aende akauze, nauli peke yake shilingi 20,000? Hii mimi naona kwa kweli kwa upande wetu halina afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata maghala hayapo, mnataka mtu anafanya implementation kuhakikisha kwamba anatekeleza agizo la Mheshimiwa Rais lengo amfurahishe Mheshimiwa Rais lakini halijamsaidia Mheshimiwa Rais kwa sababu anaowafanyia vile ni wananchi ambao Mheshimiwa Rais mwaka 2025 tunategemea kwamba ataingia uwanjani na wale wananchi tunatakiwa kupata kura kwa ajili yake. Naomba Mheshimiwa Bashe kama unanisikilza hili suala halina afya kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna budi kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake lakini ndani ya hivyo hivyo vitu pia, ndani ya vitu ambayo wanavifanya changamoto bado zipo ndiyo kama hizi ambazo tunazieleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa haya machache naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Naibu Spika, sana kwa kunipa nafasi kuchangia katika Wizara hii japo nimeona malalamiko mengi sana ya Wabunge kuhusu suala la barabara na kuna uwezekano mkubwa sana Serikali ikawa haina bajeti kubwa kwa ajili ya barabara lakini inawezekana pia ikawa hawajajipanga vizuri kwenye mgawanyo kwa ajili ya barabara hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie barabara za upande wa jimbo langu; kuna barabara ya kutoka Ifakara - Ulanga kujengwa kwa kiwango cha lami, imekuwa bingwa kuongoza kutajwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Tayari imeshafanyiwa upembuzi yakinifu lakini mpaka leo hii sijaona hata kilometa moja ambayo imetengewa barabara ile ili wananchi wangu wa Ulanga waweze kupata barabara ya lami. Hata kama ni kwa kilometa chache basi mgawanyo ule ungezingatia kidogo kuona kwamba watu wengi wana uhitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Mbunge mwenzangu jana alitaka kuruka sarakasi hapa kuona kwamba kuna mtu ana lami anaomba bajeti ya kurekebishiwa lami yake wakati sisi wengine hatuna lami na hatujawahi hata kuiona. Sijui huwa wanatumia vigezo gani, kiukweli inaumiza sana.
(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuja na special case kabisa, kwenye jimbo langu kuna daraja liko kwenye Kijiji cha Ikangao ambayo inaunganisha Kata mbili za Ilonga na Ketakeli. Daraja lile limekatika na linahudumia zaidi ya watu 28,000 na wanafanya shughuli za maendeleo ikiwemo ni pamoja na kilimo. Watu wale mwaka jana walilima ufuta walikuwa wanauza Sh.3,000 kwa kilo, baada ya daraja lile kukatika wakawa wanauza ufuta kwa shilingi 1,500.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapozungumzia suala la kilimo ni lazima tujue kwamba bila barabara hakuna kilimo ambacho kitaenda kwa sababu mazao yale hayawezi kufika sokoni kabisa. Naomba sana Mheshimiwa Waziri mara Bunge litakapoisha nifanye naye ziara kwenye jimbo langu kwa sababu jimbo lile limesahaulika kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri yupo hapa, naomba daraja hili liende likajengwe, mimi sitaki kujua fedha zitatoka TARURA au TANROADS.

Naomba wananchi wangu wakajengewe daraja hili kwa sababu lisipojengwa tena mwaka huu ina maana biashara zitakuwa zimekufa na wale wananchi mwaka ujao inawezekana wasilime kabisa kwa sababu hawana wanakoweza kupeleka bidhaa zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tutaendeleza sana kudumaza uchumi wa nchi hii kama hatutazingatia suala la barabara. Barabara ni muhimu sana, huwezi kuzungumzia viwanda kama hujazungumiza barabara, huwezi kuzungumzia kilimo kama hujazungumzia barabara. Kwa hiyo, mimi niwaombe sana, inawezekana kweli Wabunge wengi wamelalamikia suala la barabara, kuna uwezekano kwamba mkatakiwa kwenda kujipanga vizuri lakini pia hata kama mkienda kujipanga naomba sana daraja hili lipewe kipaumbele ili wananchi hawa waweze kuendelea shughuli zao za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna madaraja mengine ambapo wananchi tumejipanga kwenda kufanya kazi wenyewe kujenga daraja lile kwa sababu watu wanakufa kwa ajili ya kuliwa na mamba. Tumesema tutaenda kufanya kazi na wananchi wangu kwa kuweka hata daraja la mbao ili waweze kuendelea na shughuli zao lakini hili ni daraja kubwa sana ambalo linaunganisha watu wengi sana. Hawa nimezungumzia wananchi wachache 28,000 kutoka kwenye hizi kata mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuchangia. (Makofi)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye mpango huu wa bajeti. Pia namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kufika hapa siku ya leo. Pia nisiwe mchoyo wa fadhila, bila kumshukuru Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya ya kuhakikisha anaiendesha nchi hii katika usawa na utawala bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo kama matatu ya kuchangia kwenye Bajeti. La kwanza nitagusa kwenye mambo ya barabara. Kwanza niwapongeze Wizara zote kwa kazi nzuri wanazozifanya. Pia nawapongeza Wizara ya Ujenzi inavyopambana, tumeona miradi mingi ambayo inatekelezwa, miradi ambayo imekamilika, lakini hatuwezi kurudi nyuma maana miundombinu ya barabara ndiyo chachu ya maendeleo ya nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana niliuliza swali hapa Bungeni kuhusu barabara zetu hasa kwenye Jimbo langu la Ulanga. Majibu ya Mheshimiwa Waziri yalikuwa ni mepesi, lakini sijui ni kwa sababu gani? Kikubwa, ninapozungumzia barabara ya kutoka Kilombero kwenda Ulanga ya kiwango cha lami yenye urefu wa Kilometa 67 ilikuwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2015, lakini iliingia kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya Mwaka 2020. Bajeti zote; mwaka 2020/2021, 2021/2022 na 2022/2023 tumekosekana. Tuna imani labda bajeti ijayo tunaweza tukaingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sababu ya msingi kuombea barabara ile. Jimbo la Ulanga sasa hivi ni kitovu cha madini na pia ndiyo Mkoa wa Madini ambao Mheshimiwa Dotto alikuja kuufungua juzi. Tuna miradi mikubwa sana ambayo inakwenda kufanyika kwenye jimbo lile. Wawekezaji wanaenda kuweka zaidi ya Dola milioni 200. Sasa hivi wako kwenye mchakato wa kulipa fidia kwa wanakijiji ili kuweza kupisha miradi ile. Barabara zetu sasa hivi tunapitisha Noah tu; na gari kubwa inayopita ni Fuso, lakini ikinyesha mvua network inakatika kwa maana hiyo barabara haipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshajiuliza hivi hawa wawekezaji tusipowawekea mazingira mazuri, kesho wakianza kukafanya mobilization: Je, watawezaje kufanya kazi yao na biashara yao inafanyika masika na kiangazi? Inamaanisha adha kubwa itaenda kuwakuta wananchi wa Jimbo la Ulanga, na pia wawekezaji wale watakuwa kwenye wakati mgumu sana wa kufanya kazi yao. Hiyo ni kampuni moja nimezungumzia, Jimbo la Ulanga tunaenda kufanya makubaliano na kampuni nyingine mbili ambazo zinaenda kuchimba madini ya Kinywe. Madini haya yanaenda kubebwa kwenye magari makubwa. Barabara ile haitaweza kukidhi na kuwasaidia wawekezaji hawa kuweza kufanya kazi zao kwa urahisi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninapozungumza, nipo hapa na ndugu yangu Mheshimiwa Taletale anakuja, ametoka kunilalamikia suala la barabara. Nikamwambia mimi sio Waziri, Mheshimiwa Taletale, ongea na Mheshimiwa Waziri, mimi mwenyewe nina majanga yangu kibao jimboni kwangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara zetu Mawaziri hawa wanatakiwa watupe kipaumbele sana. Sijui kama kuna mawasiliano katika hizi Wizara. Mheshimiwa Dotto ameshamaliza kazi yake kwenye upande wa madini, kwamba watu wanaenda kufanya kazi zao. Kungekuwa na mawasiliano basi, kwamba jamani, tumeshamalizana na hawa watu wanakuja kuwekeza, waende kwa Waziri wa Ujenzi, jamani, barabara zetu zikoje? Zinaweza kukidhi mahitaji ya wawekezaji? Au hospitali, kwamba watu wanakuja kuajiriwa zaidi ya 1,000, je, hospitali zetu zinakidhi mahitaji ya watu na kuwekeza? Siyo mradi mdogo, watu wanakwenda kuwekeza zaidi ya Dola milioni 200 halafu hamna barabara, hakuna hospitali za maana, tutaenda kuchekesha, na hata hao wawekezaji watatuona hatuko serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine nirudi kwenye Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia. Ndugu yangu Mheshimiwa Francis hapa amesema, nami ilikuwa katika mpango wangu wa kuchangia leo; unamwambiaje mwananchi huyu? Kwanza unamwambia akinunua kifurushi cha siku, kwa wiki atatumia shilingi 10,000; akinunua cha wiki atatumia shilingi 5,000. Maana yake huyu mtu umemhamasisha kwamba anunue kifurushi cha wiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yetu coverage network yake ni mbaya, vijiji vingi havina network na maeneo mengi hayana network. Mkulima amejiunga kifurushi chake cha shilingi 5,000, ameenda zake shambani, baada ya siku nne anakuja mjini anaambiwa kifurushi chake kimeisha. Kifurushi chake kimeenda wapi? Hela yangu nani amekula? Tusijibizane majibu rahisi rahisi, ni lazima watu tujue kwamba hii ni dalili ya wizi watu wanaibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumlazimisha mtu anunue kifurushi cha shilingi 35,000 anatumia wiki mbili, wiki mbili nyingine unamwambia kifurushi chako kimeisha, mimi sioni kama ni sahihi na Waziri yuko hapa anatusikiliza. Tuna jambo la kufanya kwenye hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, namalizia sekunde thelathini.

MWENYEKITI: Hizo ni za mwenzio. Haya, malizia.

MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye mawasiliano na teknolojia, tuone sababu za msingi za kufunga kamera kwenye miji yetu mikubwa kwa ajili ya Security. Wenzetu Kenya wameshafunga kamera miaka saba iliyopita, sisi population inaongezeka, uhalifu unaongezeka, tunawatuma askari wanaenda porini hawajui hata mhalifu yuko wapi? Hili ni jambo la msingi sana, miji yetu mikubwa ikafungwe kamera kwa ajili ya security. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Bunge lako Tukufu. Kwanza pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya ya kuweza kusimama na kuweza kuchangia kwenye Wizara ya Afya. Pia nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kazi anayofanya. Anafanya kazi kubwa sana. Kiukweli tumpongeze, anafanya kazi kubwa, ameweza sana kuwekeza kwenye Wizara ya Afya na ameweka pesa nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Ummy, amejaribu sana kujibu maswali yangu kwenye hotuba yake, lakini naamini kwamba itaenda kufanya kazi vizuri zaidi. Kiukweli Wabunge wengi ambao wakisimama hapa kuchangia hawatakosa kutaja vitu vitatu tu ambavyo vinawaathiri Watanzania kwenye suala la afya. Hatuwezi kujenga Taifa lenye uchumi mkubwa kama watu wetu hawana afya ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kila anayesimama hapa, changamoto ya kwanza atakwambia ni dawa, changamoto ya pili atakwambia vifaatiba na changamoto ya tatu atakwambia upungufu wa watumishi. Hatuwezi kukwepa. Mheshimiwa Ummy nikwambie, huwezi kukwepa hilo, unatakiwa uende ukafanye kazi kubwa sana kwa kushirikiana na Naibu wako. Kwa sababu ukitoa mfano kwenye jimbo langu, nina deficit ya wafanyakazi wa utumishi wa afya asilimia 67. Mbunge mwenzangu aliyepita hapa amesema anao watumishi asilimia 22, kwa maana maana deficit ni asilimia 78. Ukipiga hesabu kwenye nchi nzima, inawezekana deficit ikawa asilimia zaidi ya 60 watumishi wa afya hamna. Hatuwezi kufika.

Mheshimiwa Spika, ukizungumzia kwenye suala la vifaatiba, vifaatiba hakuna. Jimboni kwangu kuna X-Ray ya miaka 20 na zaidi haifanyi tena kazi, tumehangaika kuitengeneza na Mkurugenzi wangu wa Wilaya zaidi ya mwaka mzima, imeshindikana kabisa. Hakuna taasisi yoyote inayotoa huduma ya mionzi kwenye jimbo langu.

Mheshimiwa Spika, wananchi wanatakiwa waende kilometa 75 wilaya nyingine kupata huduma ya mionzi kwa maana ya X-Ray. Huyu mwananchi ataweza wapi ku-afford hiyo gharama? Gharama ya X-Ray ni Shilingi 10,000/=. Nauli Shilingi 10,000/= kwenda, kurudi Shilingi 10,000/=, hajala, huyo mtu hawezi kufanya hivyo vitu. Tunaomba sana Mheshimiwa uende ukalifanyie kazi. Nafikiri kwenye ofisi yako nina maombi ya X-Ray muda mrefu sana. Naomba pia hilo uende ukalifanyie kazi.

Mheshimiwa Spika, hatuna ambulance kwenye Jimbo langu. Ukiwauliza Wabunge wengi hapa watakuwa wamenunua vigari kwa ajili ya kusaidia wananchi wao kama ambulance, na ndiyo ukweli ulivyo. Ina maana vifaatiba bado havitoshi. Changamoto bado ni kubwa! Hizi changamoto tatu ni lazima ukazifanyie kazi, vinginevyo hatuwezi kujenga Taifa lenye uchumi mkubwa kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Spika, lingine lazima niseme, nilileta tena maombi kwenu kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya yangu ya Ulanga. Hospitali hii hali yake ni mbaya sana. Ukienda maabara ya Hospitali ya Wilaya ya Ulanga, unaweza kusema labda hiki ni chumba na sebule ya Manzese. Ni kitu ambacho kinawakwaza sana wananchi. Miaka sita iliyopita tulipata pesa kwa ajili ya kufanya ukarabati wa hospitali ile. Hospitali imejengwa enzi ya mkoloni, lakini kila ilipokuwa inaguswa kwa ajili ya kufanyiwa ukarabati, ilikuwa haiwezekani, inaharibika zaidi. Wakafanya maamuzi ya kujenga majengo mengine. Sasa ardhi imejaa, hospitali imejaa, haiwezekani tena kwenda kuongelea majengo.

Mheshimiwa Spika, sisi ardhi tunayo, tunaomba mtujengee Hospitali yetu ya Wilaya ili tuweze kupata huduma bora. Kiukweli kuendelea kujenga Zahanati na Vituo vya Afya, kama hatuna huduma za kutosha ni sawa sawa tutakuwa tumejenga magofu, hali ya afya bado ni ngumu. Fanya tathmini ya Wabunge wote wanaochangia hapa ndani, hizi ndiyo changamoto wanazozitaja. Vinginevyo ni kwa sababu tunatakiwa tuendelee kuchangia, lakini vinginevyo changamoto zako ambazo unatakiwa kwenda kuzifanyia kazi Mheshimiwa Waziri zote zinatamkwa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto kubwa sana kwenye dawa. Inawezekana kuna tatizo MSD na Serikali, sijui ni ipi, lakini inawezekana kuna tatizo. Mwingine amezungumzia suala la wizi. Wizi kweli haukwepeki. Ni lazima tunapotoa hizi fedha tuangalie na mfumo wa udhibiti wa dawa. Ni lazima tuangalie mfumo wa udhibiti, ni mbaya mno. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Hospitali yangu ya Wilaya mwaka 2010 population ya watu ilikuwa 150,000. Ndani ya miaka 10 tu leo tunaenda kuzungumzia watu 200,000, bado hospitali ni ile ile ya mwaka 1970, hatuwezi kufika. Tunaendelea sana kujitahidi na tunampongeza sana Mheshimiwa Rais, lakini tunambebesha tena huu mzigo mwingine, bado huduma ya afya siyo salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda vijijini ukianza kuzungumzia suala la Bima ya Afya, wanakijiji wanaweza wakakutukana matusi. Hawaelewi suala la huduma ya Bima ya Afya, kwa sababu anabeba kadi yake, akienda hospitalini hapati huduma. Bado utamshawishi huyo mtu akate bima! Ya nini?

Yaani umeenda hospitalini na kadi yako na unaambiwa dawa hamna. Hakuna sababu. Kwa hiyo, wananchi hao pia kuzungumza nao kuhusu kuwashawishi kukata huduma za bima, inakuwa ni vigumu sana kwa sababu ni wagumu pia kuelewa pia kwamba kweli wakienda na hizo kadi wanaweza kupata huduma katika hospitali.

Mheshimiwa Spika, haya niliyozungumza ndiyo changamoto ya Tanzania yetu. Mheshimiwa Waziri naomba uyapokee, uyafanyie kazi. Vile vile napenda sana utembelee kwenye jimbo langu baada ya Mkutano huu kuahirishwa ili ukajionee haya ambayo nimekwambia.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kuunga mkona hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Bunge hii Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kufika hapa leo nikiwa hai, salama salmini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, na wasaidizi wake pamoja na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Imeweza kusimamia vyema kabisa na tunaona mambo yakiwa yanakwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitachangia katika sehemu mbili tatu, lakini nianze kwenye upande wa afya. Tumeona ambavyo bajeti imeongezeka kwenye Wizara ya Afya, lakini tumeona jinsi ambavyo Serikali yetu imeweza kuongeza vituo vya afya, hospitali pamoja na zahanati kwa wingi sana. Hatuna budi kupongeza hilo, hatuna budi pia kuchangia au kutoa mawazo yetu kwenye sekta ya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kweli tuna vituo vya afya vingi sana, pia tuna zahanati nyingi pamoja na hospitali. Lakini tuseme ukweli, huduma za afya bado hazijatengamaa, hazijawa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila Mbunge atakayekuwa anachangia humu ndani atakuwa anajua na atakuwa anajua changamoto ya jimboni kwake. Kikubwa zaidi watumishi wa afya kwenye hospitali zetu au kwenye zahanati zetu bado ni hafifu, japo Serikali imeajiri lakini bado. Ni lazima Serikali itupe jicho la tatu kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia dawa bado ni changamoto, wananchi wetu tunawahamasisha wakate bima za afya lakini dawa bado ni changamoto. Lakini vifaa tiba bado ni changamoto kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nikumbushe tena, ni mara yangu ya pili nachangia kwenye Bunge hili, niliwahi kusema Jimbo langu la Ulanga kuna changamoto kubwa ya afya kwa sababu hospitali ya wilaya imekuwa ndogo, lakini pia ongezeko la watu limekuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kupata wawekezaji wengi kwenye Jimbo la Ulanga. Leo tutashindwa kuhudumia kwenye sekta ya afya, waende kwenye wilaya nyingine au waende mkoani kwenda kutibiwa, tutaonekana kwamba sisi pia hatuko serious. Kwa hiyo, naomba mlichukue hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana baada ya Bunge hili kuisha, ningependa sana Waziri wa afya aje jimboni ili aje kujionea haya ambayo nazungumza. Leo ni mara ya pili au ya tatu nazungumza hapa Bungeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Madini; kuna maamuzi yalitoka ya kuhamishia biashara ya tanzanite kwenda kufanyika Mererani. Niseme ukweli kabisa maamuzi yale hayakuwa sahihi, na mtu mzima akivuliwa nguo huchutama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ruhusuni biashara ya tanzanite ifanye Watanzania wale mazao ya nchi yao. Maamuzi yale yalikuwa yanakwenda kuwanufaisha watu wachache sana, na wengi wao siyo Watanzania. Leo hii unakwenda kuacha biashara ikafanyike sehemu moja wanufaike watu wachache na wakati sekta hii imeajiri zaidi ya watu milioni sita kwenye nchi nzima. Iruhusuni biashara ya tanzanite ifanyike kwa uhuru ili watu wale matunda ya nchi yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nichangia kwenye upande wa leseni zetu za brokers; kama ambavyo nimesema, nchi hii imewaajiri watu zaidi ya milioni sita kwenye sekta ya madini, lakini leo hii ukienda kwenye upande wa ma-broker, tunajua ni wale watu wa kati ambao huwa hawana mitaji – wameweka leseni ni dola 100, watu wale hawawezi, hawana uwezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tufanye tu mahesabu kama Wahindi. Mhindi anaweka faida ya shilingi 100 anauza bidhaa zake 200 kwa siku, sisi tunalazimisha hapa tunaweka faida ya shilingi 300 unauza bidhaa 10 kwa siku. Ni mahesabu madogo hayahitaji hata degree. Punguzeni bei ya leseni watu wakate leseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, natoka kwenye jimbo ambalo yanatoka madini. Unakuta wenye leseni kubwa wako 60, halafu ma-broker ambao ni wengi zaidi, wako chini ya 50. Maana yake ni kwamba anashindwa ku-afford kukata leseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbaya zaidi unarudi upande wa TRA na wenyewe wanawakadiria kodi zaidi ya 400,000, 500,000 kwa mwaka; watu hawawezi kufanya biashara. Ukiwaangalia hata kula yao ya chakula cha mchana inakuwa ni ngumu. Kwa hiyo, nafikiri kama Mheshimiwa Waziri angekuwa ananisikia, angeweza kuwasiliana na Wizara ya Fedha kuhakikisha kwamba TRA wanaweka viwango ambavyo wananchi wale wanaweza ku-afford kufanya vile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leseni zetu kutoka kwenye dola 100, wekeni hata dola 50, hata dola 30, watu wengi watakata leseni na tutapata faida, lengo ni kukusanya mapato. Ukikatisha watu wengi zaidi utapata hela, ukikatisha watu wachache utapata hela kidogo. Kwa hiyo, ni hesabu ambayo haihitaji degree. Ni watu tu kujipanga na kuweza kufanya mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninapenda kuchangia kwenye Wizara ya Ardhi. Kwenye mijadala hapa Wabunge wamepiga kelele sana kuhusu migogoro ya ardhi, naamini Serikali imechukua na inakwenda kuifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado kuna changamoto kwenye upande wa uthamini. Ni kweli Mheshimiwa Rais kisheria anayo haki ya kuchukua ardhi ya mtu yeyote sehemu yoyote kwa manufaa ya Umma, kwa ajili ya maendelezo ya Umma. Lakini kuna taratibu ambazo zimewekwa juu ya ulipaji fidia za wale watu ambao wanataka kuhamishwa kwa ajili ya maendeleo ya Umma kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sheria inasema kwamba ukiwa umekwenda kufanya fidia, umemaliza kufanya fidia kwa wananchi, inatakiwa kulipwa ndani ya miezi sita. Baada ya miezi sita valuation inakuwa ime-expire. Sasa ikisha-expire maana yake ni kwamba unatakiwa wewe umlipe fidia ya usumbufu yule mwananchi, yule mwananchi anakuwa halipwi fidia, baada ya muda, anakuja tena mtu yuleyule anataka kufanya tena valuation upya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hajalipa fidia, mbaya zaidi haji na jedwali ambalo liko kwenye bei ya soko ya muda huo, anakuja na jedwali la mwaka 2015, leo mwaka 2023, mdizi uliuwa unauzwa shilingi 2,000, leo anataka kumfanyia valuation mwananchi yuleyule kwa bei ya shilingi 2,000, kitu ambacho…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. SALIM A. HASHAM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Bunge lako lakini pia namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya ya kuweza kusimama tena kwenye Bunge lako Tukufu kuchangia kwenye Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Spika, pia niwashukuru sana nani wapongeze, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoifanya lakini pamoja na kwamba anafanyakazi kubwa sisi Wabunge humu ndani hatutaacha kusema kwasababu changamoto bado ni nyingi na sisi humu wote tunawawakilisha wananchi zaidi ya milioni 60. Kwa hiyo, tupo kwaajili ya kuwasemea wao kwa hiyo, tutaendelea kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara yangu ya Ifakara kwenda Mahenge yenye urefu wa kilometa 68 ilifanyiwa upembuzi yakinifu mwaka 2013 na ikaingizwa kwenye Ilani ya Chama mwaka 2015 miaka mitano ile ilipita bila mafanikio yoyote na mwaka 2020 pia ikaingizwa kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi tunaangalia ndani ya miaka mitano hii Mheshimiwa Mbarawa utakuja kutufanyia nini.

Mheshimiwa Spika, kiukweli kilio cha barabara ya Mahenge – Ifakara yenye kilometa 67 ni kilio kikubwa sana kwa wananchi wa Ulanga sisi tunaokaa jimboni kwa muda mrefu ndiyo tunajua adha yake ikifika masika ukisikia barabara sehemu imekatika watu hawapiti inamaana na wewe Mheshimiwa Mbunge hata kama unasafari zako huwezi kupita kwasababu huna cha kuwaambia wananchi wako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukifika pale cha kwanza wao wataanza matusi yao watasema tu Mheshimiwa Mbunge yupo tumemchagua analala tu Bungeni. Sisi kila siku kazi yetu ni kuwasemea wananchi hawa tunaomba Mheshimiwa Waziri mtuangalie barabara ile kama mwaka huu kwenye hotuba yako utakuja kututaja na sisi tutakushukuru sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Morogoro ni Mkoa wa kimkakati na kila kiongozi mkubwa wazee wetu wangekuwa mzee wangu Kabudi hapa angesimama angeweza kuuelezea Mkoa wa Morogoro kwa upana sana. Mkoa wa Morogoro ni Mkoa wa kimkakati, Mkoa wa Morogoro umeme unaotumika Dar es Salaam unatoka Mkoa wa Morogoro lakini Mkoa wa Morogoro ndipo ambapo kuna kiwanda kikubwa cha sukari, Mkoa wa Morogoro watu wanalima kwelikweli lakini Mheshimiwa Kabudi anaujua sana Mkoa wa Morogoro lakini Mkoa wa Morogoro bado tumesahaulika sana. Sisi mpaka leo wilaya zetu hazijaunganishwa kwa lami wala mikoa yetu haijaunganishwa kwa lami kuna barabara tatu tu Mheshimiwa Waziri za kimkakati kwenye Mkoa wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, barabara ya kwanza ni ya Mahenge kwenda kutokea Liwale ambayo inaunganisha mikoa ya kusini kwa maana tutakuwa na uwezo wa kufika haifiki kilometa 100 Mheshimiwa Waziri tunao uwezo wa kufika Lindi, Mtwara na sehemu zingine huko lakini barabara ya pili ni barabara Malinyi kwenda kutokea Songea ambayo tutakuwa tumeutoboa Mkoa wa Morogoro ambayo imeanza kujengwa tangu enzi ya Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ndiyo alikuwa ameizindua barabara ile lakini mpaka leo hatujui muendelezo wake ni nini. Barabara ya tatu Mheshimiwa Waziri ni barabara ya Mlimba kwenda Njombe ni barabara za kimkakati mkitusaidia barabara hizi mtakuwa mmetusaidia sana Mkoa wa Morogoro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wilaya zetu zote hazina lami kwa hiyo, tunawaomba sana Mheshimiwa Waziri na Mama yetu anatusikiliza Mkoa wa Morogoro ni Mkoa wa Kimkakati mkoa ule una mambo mengi sana ni muhimu katika Taifa hili kwa hiyo, tunawaomba sana mtujengee barabara yetu tunashukuru barabara ya Kilombero kwenda Ifakara inaendelea kwa kasi na inaendelea kujengwa mkituunganisha na zile 67 pale sisi tutakuwa tumepona sana.

Mheshimiwa Spika, pia wewe ni shahidi mwaka jana Serikali ilisaini mkataba na kampuni moja kubwa sana ya uchimbaji inaenda kufanya uchimbaji kwenye jimbo langu imeenda kuwekeza zaidi ya dola milioni 200 kwenye lile jimbo ile kazi inaenda kufanyika pale kama barabara haitatengenezwa ule mradi hauwezi kufanikiwa kwasababu magari yatakayokuwa yanapita pale ni magari makubwa tunawaomba sana muende mtusimamie hilo muweze kwenda kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)