Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Paulina Daniel Nahato (13 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona na kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia. Napenda kumshukuru Mungu sana kwasababu ni mara yngu ya kwanza kuwa katika Bunge hili na kuchangia hotuba ya Rais. Hotuba ya Rais hii nimeipitia yote na ni hotuba yenye maono mazuri sana, yenye mwelekeo mzuri, iliyosheheni kila aina ya maendeleo ambao wananchi wowote wangehitaji kuwa nayo katika nchi yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli amejipambanua katika Afrika kuwa Rais ambaye ni wa peke sana, vyombo vya habari vimekuwa vikimsema sana kwa muda mfupi na haijawahi kutokea kwa Rais kama yeye kusemwa na nchi mbalimbali. Hiyo ni dalili tosha kwamba ameleta mabadiliko ya kutosha na tumeona katika miaka hii mitano akiwa anashughulikia nyanja mbalimbali japokuwa yeye kama alivyokwisha kusema mtu mmoja ni msomi katika eneo moja. Lakini amekuwa mtaalam katika maeneo yote karibu ya nchi yetu hii. Kwa hiyo, pongezi nyingi sana nazitoa kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile kwa safari hii pia napenda kumshukuru sana kwa sababu ukiangalia hata baraza lake la Mawaziri wengi tulitegemea, wakati bahasha inaletwa Waziri Mkuu nilijua atarudi yuleyule. Kwa sababu kwa kazi aliyoifanya Mheshimiwa Kassim Majaliwa nilitegemea tu angerudi, na wengine nilijua watarudi na wamerudi kweli. Kwa hiyo, ninamuona kabisa kwamba Rais amewaamini na hata wale ambao wengine wamefanya kazi pamoja naye amewaamini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nichangie suala la elimu. Elimu imetolewa sasa ni bure kuanzia darasa la kwanza mpaka form four na hii imesaidia sana katika kupunguza mambo mengi. Kwa mfano tulikuwa na wasichana wengi waliokuwa wanamaliza darasa la saba, uwezo wa wazazi wao ulikuwa ni wa chini ndio walikuwa wanategemewa kuwa ma-house girl katika sehemu mbalimbali na kwa kweli hawa walikuwa wananyanyasika sana, ma-house girl wengine walikuwa wanapata mishahara midogo na mwisho walikuwa wanaishia tu katika kuhangaika, lakini sasa hivi katika umri huo wa utoto wengi watakuwa shule, kwa hiyo, hayo ni mafanikio makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, vilevile hata upatikanaji wa mimba kwa watoto wa kike utashuka sana kwa sababu umri huo wa watoto wa chini ya miaka 18 watakuwa mashuleni, kwa hiyo, hii elimu bure itakuwa na faida kubwa sana. Lakini vilevile hata vijana wa kiume ambao wengi walikuwa wanajiingiza katika makundi makundi ya kuwa wezi na wadokozi, sasa nao watakuwa shule, kwa hiyo, baadae watakuwa wakubwa na watakuwa ni wa kuwajielewa.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni katika upande wa afya, afya pia imeamirika sana kulikuwa kuna changamoto sana ya wananchi hasa ya kinamama kuogopa kwenda hospitali na kwenda kwa waganga wa kienyeji kwenda kupata tiba huko kwa sababu walikuwa wakifika hospitalini walikuwa wanapata changamoto. Lakini kutokana na Chama cha Mapinduzi ambacho kimeongeza hospitali nyingi hadi kufikia katika vijiji sasa imebaki kazi moja kuwahamasisha wananchi wote kuzitumia hizi huduma afya na kubadilisha mtizamo ule wa kuamini maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, changamoto ambayo pia ninaweza labda nikaiona je, Serikali sasa iweze kujikita katika kuwasaidia wananchi katika kubadilisha mtazamo, kubadilisha mtazamo ni jambo ambalo ni gumu kitu mtu anachokiamini tangu amezaliwa ni ngumu hospitali inaweza ikawepo, dawa zikawepo, wahudumu wakawepo lakini bado mtu asiende kule kwa sababu zake binafsi labda alihaminishwa kwamba hospitali sio sehemu sahihi ya kwenda ukienda kwa mtu fulani ndiyo atakayekuhudumia au hasa katika wazazi unakuta mama mjamzito haendi kwenda kujifungua hospitalini au anakwenda hospitalini baada ya hatua imeshafikia mbaya na mwisho wake ndio vile vifo vichache ambavyo tunavisema wakati ambapo huyu mama kama angeweza kwenda mapema angeweza kupata huduma ambayo ni sahihi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa ni kazi yetu sisi kuweza kuhamasisha wananchi wetu kuanzia chini kabisa kubadili tabia zao ili kuweza kuepuka magonjwa yale ambayo yanaweza kuzuilika na kuzitumia huduma zetu za afya ili waweze kupata afya njema na kuweza kupona magonjwa ambayo yanazuilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukitizama katika Dira ya Maendeleo ya 2025 pamoja na masuala mengi ambayo yameongelewa tunazungumzia juu ya elimu bora kwa wasomi wetu wa vyuo vikuu ili tuweze kupata Taifa bora lakini sasa katika elimu hiyo ya vyuo vikuu tunaona kwamba kuna maeneo ambayo tunatakiwa kuyazingatia. Eneo la kwanza ambalo tunatakiwa kuzingatia zaidi ni teknolojia ya ufundishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli kabisa kwamba kulingana na idadi ya wanafunzi ambao tunao katika vyuo vikuu vyetu mbalimbali, ili kuweza kuwafikia wanafunzi wote ni lazima teknolojia ya mawasiiliano iboreshwe kwa sababu sio rahisi wanafunzi wote kukaa darasani kwa wakati mmoja. Bado eneo hili la elimu ya masafa marefu halijatiliwa mkazo na mfumo huu kimsingi ungeweza kupunguza gharama hata za ada kwa wanafunzi kwa kuwa wanafunzi hao wanaweza wakasoma hata wanapokuwa sehemu mbalimbali katika mikoa yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia upo umuhimu wa kuboresha ufundishaji kwa vitendo. Ukiangalia sasa hivi tumeboresha zaidi kujenga majengo kama mabweni lakini katika ufundishaji wa vitendo, hususan katika fani ya sayansi na teknolojia, Serikali iweke kipaumbele katika kuhakikisha vifaa hivyo vinapatikana katika university zetu zote. Pia ipo haja ya kuhakikisha vyuo vinapanua uwezo wake wa kufundisha wanafunzi kwa kutumia teknolojia na uwezo ambao utaongeza wanafunzi kuwa wengi katika vyuo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia kuna tatizo la motisha kwa wafanyakazi. Wafanyakazi wengi ambao wapo pale hawana motisha. Walimu wengi au wahadhiri hupandishwa madaraja lakini hawalipwi stahiki zao kwa wakati. Unakuta kwamba mtu anajitahidi kufanya utafiti lakini akishapandishwa daraja hapati pesa kwa wakati na hiyo huwafanya kukata tamaa sana hasa katika eneo la utafiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, hili linaenda sambamba na kuhakikisha kuwa wale waliopandishwa madaraja wanapata motisha ili uweze kuwasaidia. Mtu anakuwa labda ni Assistant Lecturer amekuwa Lecturer au amepanda cheo amekuwa Profesa unakuta anaitwa Profesa lakini mshahara haujapanda. Kwa hiyo, mimi naishauri Serikali kwamba iweze kuangalia suala hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika masuala ya motisha kwa wafanyakazi, hasa Wahadhiri, ni pamoja na kuangalia masuala ya maeneo wanayoishi kwa mfano hata kupewa allowance za nyumba, allowance za kufanya kazi kwa muda ule wa ziada ili waweze kufanya kazi kwa motisha na madarasa pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ninaloweza kulishauri ni kwamba, sasa hivi Serikali imeongeza wanafunzi wengi sana katika vyuo vyetu na unakuta Mwalimu huyo anafundisha muda mrefu na anaweza akafundisha hata mara tatu kwa sababu wanafunzi wanaingia session tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, nafikiri pia liangaliwe zaidi ni katika suala la hili GPA, unakuta kwamba mwanafunzi amemaliza degree yake ya kwanza ana GPA nzuri lakini sasa hapati yale masomo ya kuendelea, anapofika Masters (Shahada ya Uzamili) anatakiwa apate GPA ya 4. Kwa hiyo haya masuala yote yaweze kuangaliwa ili katika elimu ya juu tuweze kutoa wanafunzi ambao ni bora na Walimu nao waweze kuwa katika mazingira mazuri...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kengele imeshagonga.

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Ahsante sana.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami pia nichangie juu ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo. Nami nitajikita katika masuala ya afya. Awali ya yote napenda sana kuishukuru na kuipongeza Serikali katika ujenzi wa miundombinu ambayo imeifanya mpaka sasa katika masuala ya afya Na marekebisho mengi yaliyofanyika katika upatikanaji wa huduma ya afya, yaani huduma ya afya imekuwa bora zaidi.

Mheshimiwa Spika, napenda kuishauri Serikali kuwa, pamoja na kwamba tuna mambo mengi sana ambayo tunayaongelea, lakini suala la afya ni muhimu sana. Ninaomba kujikita katika sehemu ya kinga. Hili eneo la kinga au preventive au public health halijaangaliwa sana, yaani halijapewa kipaumbele sana kama tiba. Mambo mengi sana yanayoongelewa ni kuhusu tiba na siyo suala la kinga.

Mheshimiwa Spika, ni ukweli ulio wazi kabisa kwamba magonjwa mengi yanazuilika. Kama tutaweza kuzuia magonjwa mengi, tutaweza kukuza uchumi; Tutapata watu ambao watakuwa na afya na wataweza kujikita katika masuala ya uchumi hasa tutakapojikita katika masuala ya kinga. Magonjwa mengi yanatibika. Magonjwa ambayo tunaita communicable diseases na non-communicable diseases, magonjwa yote tuseme.

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, ili kuweza kufanikiwa katika eneo hili, kuna mambo matatu, kwa kifupi sana naomba kuishauri Serikali. Angalau kuwe na mipango ya aina tatu; mipango ya muda mfupi, mipango ya muda wa kati na mipango ya muda mrefu. Ninapoongelea mpango wa muda mfupi ni kwamba sasa ni kweli wananchi wengi vijijini elimu haiwafikii kuhusu visababishi vya magonjwa mengi. Matokeo yake, kunakuwa na mlundikano wa wagonjwa katika hospitali zetu, ambapo kama hao wananchi wetu watafikiwa na kujua vyanzo vya magonjwa mengi ni nini, wangeweza kujizuia, na hivyo, tuta-save fedha nyingi sana na tutafanya mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa sasa hivi ni kweli elimu inatolewa, lakini inatolewa kwenye televisheni na redio ambapo vijijini watu hawana hivyo vitu. Tufanye nini? Tufanye kila njia kuhakikisha kwamba wananchi wote hasa wa vijijini wanafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ushauri wangu ni kwamba Wahudumu wa Afya wale walioko kule vijijini kule, Primary Health Care watumike kusambaza elimu ya kinga kwa wananchi wao. Watasambazaje? Ziko mbinu nyingi za kusambaza. Wale Wahudumu wanaweza wakaongea na wagonjwa asubuhi kabisa pale wanapofika kabla ya kupata huduma wakawaeleza, wale watu wakajua na hivyo wanaweza wakajikinga. Kwa mfano, magonjwa yanayotokana na maji machafu na minyoo na vitu kama hivyo, watu wanaweza wakajizuia tu. Kama ambavyo sasa hivi tumesambaza habari kuhusu Corona na watu wanajizuia.

Mheshimiwa Spika, katika Mpango wa muda wa Kati sasa, labda kuweza kuwajengea hawa Wahudumu uwezo wa kuwapatia mafunzo ya muda mfupi mfupi (short trainings) ili hata wao wenyewe wajue namna ya kuongea na wananchi kuanzia chini mpaka kwenda juu. Faida yake ni kwamba, magonjwa yatapungua. Magonjwa yakipungua hata matumizi ya dawa yatapungua.

Mheshimiwa Spika, pia katika Mpango huo huo wa muda wa kati kuna suala la kuongeza watumishi na kuongeza utafiti. Tafiti zinafanyika, wanafunzi wanakwenda field, lakini hizi tafiti zinaishia kwenye Ofisi za Kata. Maana utafiti ukifanyika, ukimaliza kufanyika, report ndogo inatolewa inafikishwa Ofisi ya Kata au ya Kijiji, lakini zile tafiti zinawekwa tu kwenye madroo. Watafiti wakirudi mara ya pili, wananchi wanasema sisi tulikuwa hatujui, hawakupewa matokeo ya zile tafiti.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali iangalie kuhakikisha kwamba haya matokeo ya tafiti wananchi wanayapata. Kwa hiyo, msisitizo uwe kwenye Serikali za Mitaa kuhakikisha kwamba tafiti zinazofanywa na watafiti zinawafikia wananchi wote hasa wale wa chini. Basi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ya Elimu.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, napenda sana kumpongeza Profesa Ndalichako, mwalimu wangu ambaye najivunia sana kumuona akiwa kwenye kiti hicho, anatosheleza. Ni mwalimu mahiri na yupo vizuri sana. Kwa hiyo, hapo alipo pamoja na Naibu Waziri wametosheleza kwa jinsi ninavyomfahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nampongeza sana kwa kuwakilisha taarifa yake nzuri sana. Nami ni mwalimu kwa hiyo mambo yote ambayo kwa kweli kama mwalimu nilikuwa nategemea yasemwe, nimeyasikia. Kwa hilo nimeburudika sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda kukushukuru sana wewe na kwa sababu muda ni mdogo naomba niende moja kwa moja kwenye uchangiaji. Kwa kuwa na shule ya wasichana ya Bunge, Kamati tumefika kuiona, ile shule ni nzuri sana na ni ya sayansi tunategemea kupata madaktari na engineers. Tuliwaona wamekuja hapa Bungeni, wanang’aa kwa hiyo tuna uhakika baada ya muda fulani tutakuwa na kada ya watalaamu wanawake wa kutosha. Hiyo ni sifa kubwa sana kwa wanawake, kwa hiyo, hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanawake tuliosoma miaka ya nyuma masomo ya sayansi yalikuwa si ya wanawake. Mwanamke akisoma masomo ya sayansi alikuwa anaonekana kama yupo tofauti na hii ilikuwa ni mtizimano fulani ambao ulikuwa umejengeka hata wanawake wenyewe tulikuwa tunaona hivyo. Juzi Rais wetu alipokuwa anahutubia alisema moja kwa moja kwamba akili ya mwanamke na mwanaume zipo sawa tofauti yetu ni masuala ya biolojia tu kwamba mwanamke anabeba mimba na anazaa mtoto na mwanaume ana mbegu ya kuweka mimba kwa mwanamke, hiyo ndiyo tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, masuala mengine yote tupo sawa kabisa kuanzia kwenye akili, kwenye matendo, hamna kazi ambayo mwanaume anafanya mwanamke hawezi kufanya, hakuna. Ni utamaduni uliojengeka tu, is a socially constructed idea. Kwa hiyo, tunapoona wanawake wanasoma sayansi hao ndiyo tunaotegemea wawe ma-engineer, watengeneze caterpillars, viwanda watakuwa wanawake wakipanda juu na kutengeneza mashine. Nataka kusema nini hapa? Nataka shule za wasichana ziongezwe hasa katika michepuo ya sayansi ili kuwe na ile notion ya zamani ambayo wengine tuliikosa katika masomo ya sayansi sasa tunapoenda kwenye fifty fifty wanaume kwa wanawake pia kwenye masuala ya sayansi tuwepo.

Mheshimiwa Spika, nini sasa tufanye ili tuweze kufikia pale? Kwa tafiti ambazo zimefanyika zinaonyesha kwamba wasichana wanapokuwa wenyewe katika shule zao, wanaposhindana wenyewe wanafanya vizuri sana. Mtakubaliana na mimi tunapoangalia zile shule ambazo zimefanya vizuri, japokuwa zipo pia na za wanaume wenyewe kwa wenyewe lakini za wanawake zinaoongoza ni zile ambazo wanawake wako wenyewe.

Mheshimiwa Spika, sijajua sababu ni kitu gani lakini mojawapo ni kwamba wanawake wanapokuwa wenyewe wanakuwa na ile hali ya kujiamini zaidi kwa sababu yale mambo ya kuona aibu na maneno maneno ambayo yalikuwa siku za nyuma yanakuwa hakuna. Kwa hiyo, wanaposhindana wenyewe kwa wenyewe kunakuwa na kujiamini.

Mheshimiwa Spika, mimi nafikiria siku zijazo angalau tufike hata kila wilaya kuwa na shule za bweni za wasichana ambazo zitakidhi mahitaji ya wasichana. Hata masuala aliyoongea Mheshimiwa mambo ya taulo za kike, ile sisi tumejisikia vibaya lakini ndiyo ukweli ila kwa vile ameongea mwanaume tukajisikia vibaya, tuondoke tu ni mwanaume kasema ni sawa.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hivyo Mheshimiwa Waziri nafikiri baadaye tutawaza kuona kwamba kila wilaya inakuwa na shule ya wasichana na itiliwe mkazo masomo ya sayansi. Ili chuo kikuu basi zile faculty zote za sayansi tuone wanaume na wanawake ili baadaye wanapoingia katika soko la viwanda wanawake wawepo wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba sasa nizungumzie suala moja la mfumo wa mikopo. Suala hili tunaishukuru Serikali kwamba sasa hivi angalau imeongeza pesa. Takwimu inaonyesha kwamba itakapofika 2525 wanafunzi watakaokuwa wanaingia shuleni ni mara mbili. Hii ina maana kwamba form four, form six na chuo kikuu wataongezeka mara mbili, tumejiandaaje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mfumo wa mikopo uliopo sasa hivi una changamoto, haupo sawa. Kuna wanafunzi ambao wanakosa mikopo, hawa wanaotoa mikopo kuna masharti ambayo wanasema ni lazima huyu kijana anayepata mkopo awe yatima, wazazi wake waonyeshe hawana uwezo na vitu kama hivyo. Sasa utawezaje kupima kwamba huyu kijana ni maskini hiyo ni kazi kubwa sana. Matokeo yake nini? Wanafunzi wanaingia chuo kikuu wanakosa mikopo na mbaya zaidi hawa wanaokosa mikopo ni wale ambao kabisa kwa ukweli ni maskini na hivyo wanashindwa kumaliza masomo yao. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Paulina Nahato.

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ili nichangie katika Wizara ya Afya. Awali ya yote napenda kumshukuru Waziri wa Afya kwa kutuwasilishia taarifa yake nzuri. Naomba nichangie katika sehemu moja tu ambayo ni elimu ya afya kwa jamii na hususani nitachangia katika sehemu ya tabia au tuna sema behavior change.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni dhahiri kabisa kwamba magonjwa mengi ambayo yanaikumba jamii yetu yanaepukika. Tatizo kubwa ni kwamba wananchi wengi hawajui na kwamba kwa sababu hawajui hata tabia zile ambazo ni tabia hatarishi ambazo zinaweka katika mazingira ya kupata magonjwa, wananchi wengi hawajui hususani wananchi wanaoishi vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, magonjwa yapo, lakini watu hawajui, hawajui kwa kiwango gani magonjwa yapo na hata kama yapo hawajui yaani hakuna ufahamu wa kutosha kuhusu aina mbalimbali za magonjwa. Magonjwa aina zote; magonjwa ya kuambukiza na yale yasiyo ya kuambukiza. Kwa hiyo, watu wanaishi tu kwa sababu hawajui, mpaka mtu anapofikia sasa anaumwa ndiyo anaanza kushtuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba niishauri Serikali kuimarisha kitengo hiki Elimu ya Afya ya Jamii (public health), watu sasa wafikie kupata taarifa sahihi kwamba magonjwa yako kwa kiasi gani. Elimu itolewe; kwanza watu wajue kuna aina gani ya magonjwa na nini kisababishi cha haya magonjwa, tuna magonjwa mengi ambayo yanayosababishwa kutoka kwa mtu, mengine ni kutokana na mawasiliano ya wanyama na watu, mengine ni wadudu wengine ya kwenda kwa watu, lakini watu hawajui. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wanaishi na Wanyama, hawajui kwamba wanyama wanaambukiza magonjwa zoonotic diseases watu hawajui na kwamba hata yale magonjwa mengine ambayo yanatokana na maziwa, watu wanakunywa maziwa bila kuchemsha, hawajui kwamba ni rahisi kupata magonjwa fulani. Kwa hiyo, kunahitajika elimu kwanza ya kujua kuna aina gani ya magonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ni kwamba pia elimu itolewe ya kutosha kuhusu watu kubadili tabia zao, tabia ambazo zinaweza kuwaweka katika mazingira hatarishi ya kupata magonjwa. Kila mtu akishajua hivyo ni rahisi kujichunga na kama mtu mmoja atajichunga basi jamii yote ni rahisi kujikuta kwamba inakuwa na uelewa wa kutosha kuhusu magonjwa. Kwa hiyo hatutalalamika sana kuhusu tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni kwamba, watu wanaweza kujua juu ya magonjwa, lakini hawajui faida za kwenda hospitali. Wengi wanakwenda hospitali wakati magonjwa mengi yameshafikia katika stage fulani ambayo ni mbali. Kwa mfano magonjwa labda ya kansa hivi, magonjwa mengine, mtu anakwenda hospitalini akifika kule unakuta imeshakwenda imefikia stage four, sasa pale ndiyo tiba inakuwa ni ghali sana, wakati ambapo huyu mtu angejua dalili za awali, akaenda hospitali huyu mtu angetumia pesa kidogo tu kwa matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo utamaduni wa tabia ya kwenda hospitalini ya kucheki afya mara kwa mara unakuwa haupo hata kwa watu wenye kipato hasa wenye kipato cha juu. Kwa hiyo matatizo haya ya ukosefu wa dawa yanakuja kwa sababu watu wanakwenda hospitali wakati tayari hali imekuwa ni mbaya. Kama ni presha imeshafika juu, kama mtu angekuwa na tabia ya kucheki afya mara kwa mara huenda angeshajigundua ana BP mapema, angechukua hatua mapema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusisitiza juu ya behavior change, kubadili tabia. Hivyo, basi vitengo katika Wizara ya Afya vijikite katika kuimarisha kubadili tabia behavior change aspect. Baada ya hii watu kujua faida zake pia wajue changamoto ambazo wanaweza kuwa nazo. Mtu akiwa na afya anaweza kwenda hata Mumbai kwenda kucheki afya yake na mtakubaliana na mimi kwamba mtu anaweza akawa anaumwa kichwa, kuumwa kichwa siyo ugonjwa, ni dalili ya ugonjwa fulani, hasa huyu mtu anaumwa kichwa anakunywa panadol anajiona yuko sawa, hafanyi mazoezi anaendelea na shughuli zake, akisikia usingizi anakwenda analala, kumbe huyu mtu ana tatizo kubwa. Anapokuja wanashangaa huyu mtu ameanguka akiletwa hospitalini, huyu mtu yuko ICU matibabu ni makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tujaribu pia kuimarisha hivi vitengo vya kuangalia tabia za watu, wajue pia ni changamoto gani watakazokumbana nazo wanapokwenda hospitali. Kwa hiyo kujengwe na hiyo tabia ya watu kucheki afya zao. Pia wanahitaji kukumbushwa mara kwa mara, watu wakumbushwe mara kwa mara. Hapa sasa siyo Wizara ya Afya tu, tunaingia Wizara ya Maji, yaani Wizarani ichanganyike na Wizara nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Michezo iwakumbushe watu faida za michezo; Wizara ya Maji iwakumbushe watu, Wizara ya Mifugo iwakumbushe watu kutokuchangamana na mifugo; na Wizara ya Uvuvi iwakumbushe watu kutokutumia yale maji ambayo ni machafu. Kwa hiyo watu wapate kukumbushwa mara kwa mara na hivi vyombo vya habari vitumike hususani television, radio, simu, mawasiliano ya mara kwa mara ili watu wakumbushwe wajue hatari na mazingira yaliyoko kwamba ni hatarishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho Wizara pia iangalie suala la kuhakikishwa kwamba watu wanabadili tabia zao na kuwa na tabia zile ambazo zitawafanya wawe na afya ambayo tunaita safe efficacy, ni muhimu sana. Kama hivi vitu vyote Wizara itaviangalia kwa macho matatu, basi uwezekano wa kupunguza magonjwa mengi katika jamii zetu utakuwa ni mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi Wabunge ni vizuri kusoma mara kwa mara ili pia tutumike kama chombo cha kufikisha ujumbe wa masuala ya afya kwa jamii. Katika mikutano yetu, tusiongelee mambo yetu ya siasa tu, tuweke kipaumbele katika elimu na sisi tupate elimu, tuwe na shauku ya kujua magonjwa, maambukizi na jinsi magonjwa yanavyokuja na hatua za magonjwa ili watu wetu katika majimbo yetu iwe ni gumzo. Itakapokua ni gumzo tutajenga jamii ambayo itakua na afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Serikali kutenga fedha za kutosha katika Idara hii ya Health Promotion and Health Education ili iweze kupata fedha za kutosha na pesa hizi zitumike katika kufikisha elimu ya afya kwa jamii ili watu waweze kuchukua hatua za kubadili tabia ambazo zinawaweka katika mazingira hatarishi ya kupata magonjwa, tutaweza kuokoa fedha nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi kuchangia katika Wizara hii. Napenda sana kuipongeza Wizara hii chini ya Waziri pamoja na mdogo wangu Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayofanya. Kwa sababu nina dakika tano mimi naomba nichangie katika eneo la utangazaji.

Mheshimiwa Spika, kama tunavyofahamu suala la utangazaji au habari; ufikishaji habari ni haki ya kila na hata katika ilani yetu ya chama pia tumejipambanua kwamba kila mwananchi ana haki ya kupata habari sahihi. Sasa nitaenda moja kwa moja kusema kwamba katika channel zetu za tv upatikanaji wa habari bado hautoshelezi na usikivu wa channel hasa channel ya TBC ni limited na kama tunavyofahamu katika maeneo ya pembezoni sehemu kama Ngorongoro ambayo ni eneo kubwa, lakini upatikanaji wa habari kwa sehemu hii kwa kweli ni hafifu na maeneo kama Namanga, maeneo kama Longido na Bukobwa zile sehemu ambazo ziko pembezoni wale wananchi hawapati habari.

Mheshimiwa Spika, habari ni muhimu sana, kwa mfano kama hotuba za Rais ni muhimu kila mwananchi akaisikia. Kwa hiyo, mimi naishauri Serikali iweze kuangalia hili kwa sababu habari ni muhimu katika kulinda nchi yetu, jambo lolote la hatari litakapotokea ni vyombo vya habari ndivyo vitakavyotumika kusambaza habari na mambo kama ujenzi wa uzalendo, mambo kama utamaduni wetu vyote hufikiwa kwa habari. Kwa hiyo usikivu wa channel ambao kwa mgano tuna channel yetu ya TBC ambayo ni asilimia 63 na ni channel ambayo ni ya Taifa tunaomba hii iwekewe mkazo iweze kufikia watu wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili kwa haraka niende kusema kwamba naiomba Wizara iangalie suala la wasanii wetu waweze kutengeneza tamthilia. Kwa sasa hivi tumejikita zaidi katika sinema zetu na unakuta hazifurahishi kwa sababu nyingi sinema ni fupi na kwa sababu hata wale wanaocheza sinema wengi wanajitegemea, hawana pesa za kutosha mtu ukiangalia filamu unajua itaishiaje.

Kwa hiyo hata hupati mvuto wowote unajua tu hii sinema imeanza climax yake itaishia hivi. Kwa hiyo haupati ile hamu ya kuangalia. Lakini filamu kama Isidingo na filamu zingine za nje ni nzuri kwa sababu zinakupa hata mtu umechoka kusikiliza.

Kwa hiyo, nilikuwa naomba Wizara iangalie kutengeneza tamthilia ndefu kama Isidingo, lakini iwe inaakisi tamaduni zetu, lugha yetu na itaweza kujenga Taifa kwa ubora na watu watakuwa na hamu ya kuiangalia mara kwa mara kwa sababu mtu hatajua inaishiaje na hivyo basi pia tutatengeneza uchumi na itaweza kuwajenga vijana kuwa na weledi wa kuweza kutengeneza filamu zenye ubora kuliko sasa hivi ambazo tunaangalia nyingi zimejielekeza katika mapenzi na mambo fulani fulani ambayo ni kwa ajili tu ya kupata kipato kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo lingine naomba kusisitiza juu ya mambo ya channel ya utalii. Channel ya utalii bado haijakaa vizuri, coverage yake bado haitoshi utalii wetu unatakiwa utangazwe sana waandishi wa habari nimepata habari walipata semina kutoka Tanzania nzima, lakini unakuta wanapokwenda kutengeneza filamu za utalii pesa haitoshi, wanakwenda katika mbuga za wanyama au sehemu mbalimbali wanakaa siku tatu. Siku tatu utatengeneza filamu gani? Haiwezekani na yote hayo ni kwa sababu ya pesa, ili utengeneze filamu nzuri inatakiwa muda na vitu vyote vile vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa kifupi siwezi nikasema lakini naomba channel hii ya utalii hata watalii wenyewe wanapokuja wakati mwingine kutokana na usikivu kuwa hafifu wanaulizia channel za utalii, mtu hajui nakumbuka mimi nilipokuwa Marekani mtalii mmoja alikuja akasema mimi nimengalia channel, lakini sijaona mlima Kilimanjaro je, wewe umeuona? Nikamwambia nimewahi kuuona, akanikumbatia, akaniambia daktari nafurahi nimemshika mtu ambaye amepanda Mlima Kilimanjaro. Lakini Mlima Kilimanjaro ungetengenezewa channel nzuri ungeweza kuleta watalii kwa wingi zaidi. (Makofi)

Kwa hiyo naomba kusisitiza kwamba hii safari channel na channel zingine ziwepo na zitengewe pesa ya kutosha ili ziwe na coverage nzuri yaku-capture utalii wetu na uweze kusambaa dunia nzima na iwe ni channel ambayo ni imara zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la mwisho sasa labda kwa ajili ya muda haraka napenda kusemea juu ya…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Paulina Nahato.

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante na naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia. Awali ya yote napenda sana kumpongeza Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya, pia napenda kuipongeza Wizara ya Maendeleo, Jinsia na Watoto pamoja na Waziri wake na Naibu kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, mchango wangu leo utajielekeza katika suala la ukatili wa watoto. Suala la ukatili kwa watoto limekuwa ni changamoto kubwa sana katika Taifa letu na limekuwa likiongezeka mara kwa mara. Kama tunavyofahamu watoto ndiyo Taifa la kesho, watoto wanaandaliwa kuanzia wanapokuwa tumboni, tangu mama anaposhika mimba na maendeleo ya mtoto pale ndiyo yanapoanza. Mimba ikiwa haitatunzwa vizuri hata ukuaji wa huyo mtoto atakapozaliwa hautakuwa mzuri. Mimba inabebwa vizuri na mwisho mtoto anazaliwa, lakini sasa anapofika duniani na kuanza maisha anakutana na changamoto. Hili ni jambo la kusikitisha sana na katika Kamati yetu ya Huduma za Jamii tumeliangalia suala hili la vitendo vya ukatili wa watoto na jinsi ambavyo linaendelea katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa takwimu za Polisi ambazo Wizara imetupatia ya mwaka 2021, inaonesha kwamba, ripoti ambazo zimeripotiwa Polisi japokuwa hizi ripoti zilizoripotiwa Polisi wote tunaamini kwamba zitakuwa siyo zote zilizoripotiwa, lakini kwa hizi chache ambazo zimeripotiwa bado zinatosha kutupatia picha halisi ya ukubwa wa hili tatizo. Kwa mfano, matukio yaliyoripotiwa jumla yake ni 11,429 ambayo hayo yametolewa taarifa katika vituo vya Polisi.

Mheshimiwa Spika, matukio yaliyotolewa taarifa ni ya ubakaji ambayo ni matukio 5,899, mimba kwa wanafunzi ni matukio 1,677 na ulawiti ni matukio 1,114 pamoja na kuzorota kwa masomo ni 790 na mashambulio ya mwili ambayo ni 350. Hizi ni zile ripoti ambazo zimeenda kuripotiwa katika vituo vya Polisi, lakini tunajua kabisa katika utamaduni wetu wa Kiafrika tofauti na tamaduni za nchi za nje ambapo mtoto hata anapopigwa kibao na mama yake anachukua simu palepale mezani na kuwapigia ustawi wa jamii na ustawi wa jamii unamchukua na kumpeleka katika vituo vya kulelea watoto na huyo mzazi hatamwona mtoto wake, hilo ni tofauti na kwetu kwa hiyo wazazi wanaogopa sana kuwafanyia ukatili watoto.

Mheshimiwa Spika, katika nchi zetu za Kiafrika na Tanzania ikiwemo, vitendo vya ukatili kwanza tafsiri yake ni ngumu, kumchapa mtoto kama Waziri Mkuu alivyosema leo na mimi pia nilikuwa nataka kusema, mimi kiboko hapana! Kiboko siyo adhabu kwangu, mtoto tiba yake ni kuongea na mtoto lakini sasa katika nchi yetu, tunaona kwamba familia hazijachukua nafasi yake. Ubakaji wa watoto takwimu zake hatuna, kwanza ubakaji umeanzia wapi kwa mtoto? Mtoto wa miaka mitatu, mtoto wa miezi sita amebakwa imeanzia wapi? Huu ni utamaduni wa wapi? Mimba za wanafunzi! Suala kubwa ambalo mimi hapa naliona ni kwamba wazazi hatujachukua nafasi zetu kuongea na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata mtoto akizaliwa tu pale unapokuwa mama unamnyonyesha, unapoongea na mtoto anakuelewa hizo ni tafiti zinavyoonyesha. Mama unapongea na mtoto na mtoto anacheka ananyonya anakuangalia unamsemesha anaelewa! Kwa hiyo, hata baadae atakapokuwa na mwaka wa kwanza na mwaka wa pili unavyoendelea kuongea naye unasogeza ukaribu wa yule mtoto, kwa hiyo inakuwa ni mwanzo wa kuwa karibu na watoto.

Mheshimiwa Spika, suala kubwa ni kuvunja ukimya kwa watoto, tutakapovunja ukimya kwa watoto, watoto wakiwa karibu hakuna jambo watakaloficha. Kama katika nchi zilizoendelea, mtoto anaweza kupiga simu yaani mama yake amempiga tu kibao kidogo tu ananyanyua simu, anamwambia mama I will call the social worker and she/he will call the social worker kwa mama yake aliyemzaa, hivi kwetu Watanzania tunakwama wapi? Tukianza kuwazoeza watoto wetu kuongea mambo mazuri tu, mambo ya kawaida, mambo ya ngono, mambo ya sehemu za siri, mambo ya vitu vingine, watoto wanaelewa na watatupa taarifa na huu ukatili mwingi utapungua. Tunakuja kusubiri mtoto amelawitiwa mara thelathini, mara arobaini mpaka ameshakubuhu, siku umemkamata ndiyo mama au baba mbio unakwenda Polisi kuripoti, hasa unaenda kuripoti nini? Baada ya muda tena, na wewe mwenyewe mzazi ni maskini unapenda pombe, unakuta tayari.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi labda napenda kusema tu, Serikali umefika muafaka wa kuchukua hatua. Tukae chini tuchukue hatua madhubuti ya kuhakikisha kwamba tunakuwa karibu na watoto na vile vile tuhakikishe tunawaweka watu ambao ni wataalamu wa kuweza kuongea na watoto pamoja na wazazi wao. Tuimarishe maongezi kati ya watoto na wazazi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili pia hizi sheria zirekebishwe. Once sheria imeshakuwa imewekwa mezani wazazi wasije wakasema aah! tumeshaelewana tunaomba tu hili la kijamii tukalimalizie nyumbani. Haya masuala ya kwenda kumalizia nyumbani yanawasababishia watoto ukatili; nao hao wakiwa wakubwa watafanya ukatili kwa watoto wao. Kwa hiyo, jamii itakuwa na mwendelezo wa ukatili miaka na miaka na haitaisha. Tukianza kuziba mwanya huku chini tutaweza kurekebisha hii tabia ya ukatili kwa Watoto.

Mheshimiwa Spika, lakini mwisho niseme kwamba, elimu itolewe hata kwa hao waathirika. Mtoto anapoathirika hili linabaki kuwa donda linabaki kwenye moyo wake na halitaisha; na ili liweze kuisha ataendelea kulipiza. Kwa hiyo, atakapokuja kuwa mtoto mvulana anaanza darasa la pili la tatu la nne atakuwa anafanya vile akifikiria kwamba anajifariji kumbe naye anaongeza tatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi napenda kuishauri Serikali hili jambo tuliangalie vizuri sana. Tusilichukulie tu ukatili, ukatili, ukatili chanzo cha ukatili ni nini kwenye jamii yetu? Na katika nchi zilizoendelea wamefanya nini kupunguza ukatili? Nchi ya Norway ambako mimi nimesoma hivi vitu havipo, na watoto wakifanyiwa hivyo hata ukimuangalia tu anakuambia why are you looking at me? Mtoto mdogo anakuambia why are looking at me? Yaani kuonesha kwamba anajielewa. Kwa hiyo, watoto wetu wa Kiafrika tuwajengee kuanzia wakiwa wadogo wajielewe, wajenge ile uwezo wa kushangaa mtu anapotaka kumwambia lolote sio hii ya kumwambia aah wewe ni mjomba, wewe ni mtoto wa kaka yangu, wewe ni mdogo wangu ngoja nikuogeshe tulale pamoja, mtotoo anaona kama ni kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tunaomba Serikali ichukue sheria kali sana na kuhakikisha kwamba elimu inatolewa ya kutosha kuweza kuhakikisha ukatili kwa watoto unaisha ili tujenge jamii inayokuja tofauti kabisa, na hii iwe ni historia ya masuala ya ukatili kwa jinsia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Dkt. Paulina nilikuwa najiuliza hapa, kwa hivyo kumchapa mtoto kibao ni ukatili?

Mheshimiwa Paulina, kumchapa mtoto kibao ni ukatili? Inabidi aende polisi? (Kicheko)

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, nimetolea mfano wa nchi zilizoendelea, lakini mimi sipendi kuchapa mtoto kwa ujumla, kibao, kiboko naona kwamba ni ukatili kwa sababu hata huo mkono utakao mchapa unaweza ukamsababishia kutokusikia maisha. Kwa hiyo, sijui labda umetoka kwenye stress zako, sio wewe Mheshimiwa, samahani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mtu ametoka kwenye pombe zake kwenye stress zake amegombezana na hawara zake anamchapa mtoto kibao, hajui ule mkono aliomchapa nao amemchapa kwa kiasi gani, atamsababishia kilema cha maisha, nilikuwa namaanisha hiyo. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia na mimi nichangie katika Wizara hii ya Sayansi, Teknolojia na Elimu. Awali ya yote napenda kumshukuru Mungu kwa kunipatia nafasi ya kusimama hapa leo na kuchangia katika Wizara hii.

Napenda pia kuchukua nafasi ya kuwapongeza Wizara ya Elimu, Waziri Profesa Mkenda pamoja na Naibu Waziri Mheshimiwa Kipanga pamoja na timu yote ya Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli Wizara ya Elimu inafanya vizuri sana. Nami pia nichukue nafasi ya kumshukuru sana Rais wetu Samia Suluhu Hassan kwa kuangalia hii sekta ya elimu na kuipa kipaumbele. Kwa hivi karibuni tumeona madarasa mengi yamejengwa na haya madarasa yaliyojengwa ni dalili kwamba sasa Vyuo vyetu Vikuu vijiandae kuwapokea wanafunzi wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kila mwanafunzi anayesoma hata kuanzia shule ya msingi ukimuuliza swali unataka kuwa nani atakwambia nataka kuwa Daktari, nataka kuwa Pilot, nataka kuwa Injinia, nataka kuwa Mwalimu lakini atakuwaje Mwalimu, mwisho wake ni wapi? Mwisho wake ni Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba hivyo basi nichangie katika eneo la Vyuo Vikuu. Katika nchi yetu ya Tanzania tuna takribani Vyuo Vikuu 34. Vyuo Vikuu 12 ni Vyuo Vikuu vya Umma, Vyuo 22 ni vya Sekta Binafsi na vilevile tuna Vyuo Vikuu vitatu na ambavyo ni Vyuo Vikuu Vishirikishi kikiwepo Chuo Kikuu Kishirikishi kilichopo Mbeya - MUST, kilichopo Iringa – MUSE na kilichopo Dar es Salaam – DUCE.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Vyuo Vikuu hivi vina Wahadhiri 7,647 na hao ndiyo Wahadhiri waliopo katika Vyuo vyetu Vikuu hivi 34. Na hao Wahadhiri wenye elimu ya Uzamivu yaani Shahada ya Uzamivu (PhD) ni 2,185 sawa sawa na asilimia 28.6. Wenye Shahada ya Uzamili (Masters) ni 3,875 ambao ni sawa sawa na asilimia 50.7 na wenye Degree ya Kwanza ni 1,587 sawa sawa na asilimia 20.8. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii idadi ya Wahadhiri ni ndogo, ukilinganisha na wanafunzi katika Vyuo Vikuu. Hii idadi ni ndogo, matokeo yake ni nini? Ndoto ya wanafunzi wanaofika Vyuo Vikuu inafifia hapa katika Chuo Kikuu. Wanafunzi hawa wamesoma kuanzia Elimu ya Msingi, Sekondari hadi wanafika Chuo Kikuu wanakutana na changamoto ya upungufu wa Wahadhiri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aliwahi kusema Mheshimiwa mmoja sehemu kwamba hata ukiwachukua wanafunzi leo ukawaweka katika hoteli ya nyota tano halafu hao wanafunzi wakapata kila kitu lakini kama Wahadhiri wa kuwafundisha hawapo ni bure. Tutapata wanafunzi ambao hawataendelea na wataondoka katika maeneo hayo, tutapata wanafunzi ambao watachanganyikiwa na mwisho wa siku hata ndoto zao hazitafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii changamoto imetokana na hii sera ya kusema Wahadhiri wanaajiriwa kutoka Utumishi, Wahadhiri wanatoka Utumishi. Kwa hiyo, kila wakati Vyuo Vikuu vinapokosa Walimu wanasema hili tatizo liko Utumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashauri kwamba kama ambavyo wengine walishashauri asubuhi, kwamba sasa Vyuo Vikuu virudushiwe ile autonomy waweze kuajiri wenyewe. Mheshimiwa Waziri Vyuo Vikuu vinawatambua wanafunzi ambao wana uwezo wa kubaki pale na kufundisha na hapo zamani ndivyo ilivyokuwa. Wanafunzi wanapokuja pale wanafanya Degree ya Kwanza, wale wanaofanya vizuri na kuwa na GPA nzuri ndiyo waliokuwa wanaajiriwa. TCU wameweka kwamba GPA ya kufundisha Chuo Kikuu japo kuwa hapo pia kuna tatizo fulani kwa sababu kwenye Vyuo Vikuu vingine wanachukua GPA 3.5 lakini Vyuo Vikuu vya Umma wamesema wachukuliwe wale wanaopata GPA ya 3.8 lakini hata hivyo siyo jambo baya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanafunzi wanamaliza wana 3.8, wana 3.9 mpaka 4.0 mpaka 4.2 lakini mwisho wake hawajui kwa sababu Utumishi hawajawaajiri na Chuo bado kina shida lakini hawana ile autonomy ya kuajiri hawa wanafunzi au kuajiri hawa wawe Tutorial Assistant na mwishowe wajiendeleze mpaka wapate Shahada ya Uzamivu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, naishauri Serikali, naishauri kwa dhati kabisa, hapa Chuo Kikuu ndiko ambako tunawatoa Wahadhiri wenyewe, hapa ndipo watumishi wa Serikali wanakotoka, maana watumishi wa Serikali wengi ni wale ambao wameshapita Chuo Kikuu, Sekta Binafsi hata wafanyabiashara wengi wangetaka wawe na Degree ili waweze kufanya biashara zao vizuri. Kwa hiyo, hili jambo naomba Wizara iliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende sasa kwenye uwiano wa kijinsia katika Vyuo Vikuu. Kati ya hao wanafunzi 7,000 kama nilivyokwisha kusema, hawa 7,647 wanaume ni 5,766 asilimia 75.4 ni wanaume. 1,881 asilimia 24.6 ni wanawake. Hivi ni kwanini? Kwani wanawake hawawezi? Kweli asilimia hii hata nusu haijafika? asilimia 75 ndiyo wanaume? Tatizo liko wapi? Hawa wanawake kwani ina maana hawawezi kweli kusoma hata kama huko nyuma hali ilikuwa tofauti? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Wizara iwaangalie wanawake, kwa sababu katika Sekondari kuna shule zinafanya vizuri za wasichana. Tatizo liko wapi wakifika Chuo Kikuu Wahadhiri wanakuwa asilimia 24 ya wanawake? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ifike mahali tufanye maamuzi magumu ya kuhakikisha kabisa hawa wanawake nao wanapatikana. Sasa mimi nina wazo, kuna hii project ya Higher Education Economic Transformation (HEET) ambayo imedhamiria katika mwaka 2021/2022 mpaka 2025/2026 kuwasomesha wanafunzi wa Degree ya Uzamivu 623 na Uzamili 477. Mimi nashauri Serikali angalau robo tatu wawe wanawake. Wanawake wote ambao wanaweza kusoma Chuo Kikuu na wanafikia vigezo vya kuwa Wahadhiri basi wapewe nafasi ya juu katika kuwafikiria. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika nchi zilizoendelea hata katika miradi iliyoko Chuo Kikuu ukipeleka mwanamke wanasema women are highly encouraged, kwa maana ya kwamba wanatambua na hata mradi unaolipa Chuo Kikuu wanasema ukipeleka candidate ambaye ni mwanamke unapewa asilimia 40 katika ile project.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mimi naiomba Serikari iangalie kuweza kuwapata Wahadhiri wengi wanawake hii pia itaondoa malalamiko. Sasa hivi tunafikiria kuweka dawati la jinsia, dawati la jinsia kwa nini? Hawa wanawake ni mama, hawa wanawake ni wanawake, wanajua matatizo ya watoto wa kike lakini sasa unakuta ni wanaume ndiyo wengi. Sasa hata tatizo likitokea kesi ya ngedere utapelekaje kwa nyani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wanaume, mwanaume kakosea, kateleza kesi inapelekwa kwa mwanaume, kwa sababu wanawake hawapo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine katika Vyuo Vikuu ni katika uongozi. Vyuo Vikuu vingi ni wanaume ndiyo wanaopewa nafasi ya uongozi. Nakipongeza sana Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Profesa Anangisye Mwalimu wangu yeye amefanya vizuri sana. Amewajali wanawake. Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kinawajali wanawake sana, na hilo nawapongeza sana Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. Mheshimiwa Waziri naomba hii jambo liingwe na Vyuo Vikuu vyote kuwaweka wanawake katika nafasi za juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nami pia naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami nichangie katika Wizara hii ya Afya. Awali ya yote, napenda kumshukuru sana Mungu kwa kunipatia nafasi nami kuweza kuchangia katika Wizara hii ya Afya. Napenda sana kumshukuru Rais wetu kwa ajili ya kumwamini Mheshimiwa Ummy Mwalimu kuwa Waziri katika Wizara hii ya Afya pamoja na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Mollel. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pasi na shaka Mheshimiwa Ummy Mwalimu ni mchapa kazi, Rais hajakosea. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, baada ya mchango kuhusu afya ya akili, sasa huyu ni mtaalamu wa afya ya akili. Kwa hiyo, tumsikilize mtaalamu wa afya ya akili akichangia. (Makofi/Kicheko)

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba muda wangu dakika moja uweze kuniongezea. Nampongeza mchangiaji aliyechangia katika masuala ya afya ya akili. Aliloliongea nami nataka kuliongezea hapo hapo.

Mheshimiwa Spika, suala la afya ya akili na magonjwa mengine kwa kweli ni changamoto. Katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya mwaka 2020, ukurasa wa 138 (w), lengo la chama chetu wakati tunainadi ilikuwa inasema hivi, nanukuu: “kutoa elimu na uhamasishaji kwa wananchi kuhusu kinga, udhibiti na kuzuia magonjwa yasiyoambikiza ikiwepo afya ya akili.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) ya mwaka 2021 inaonesha kwamba, watu takribani milioni 38 hupoteza maisha kutokana na magonjwa yasiyo ya kuambikiza ikiwepo afya ya akili. Hawa watu ni wa umri kati ya miaka 30 mpaka 69 hasa katika nchi zinazoendelea.

Mheshimiwa Spika, magonjwa yasiyoambukiza yamekuwa ni changamoto katika nchi yetu na magonjwa haya Waheshimiwa wengi waliochangia hapa wameyaelezea. Ukiangalia hata matatizo yote ya kijamii ni kutokana na magonjwa ambayo siyo ya kuambukiza ikiwemo hiyo ya afya ya akili. Magonjwa hayo ni kama shinikizo la damu, moyo, kisukari, saratani na mengine kama ya afya ya akili, kupooza, hata kutokuona vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, magonjwa haya, kama alivyotangulia kusema aliyechangia, ni ya maisha na hivyo basi tiba yake ni ghali sana. Hupoteza nguvukazi ya watu, watu hubaki na umasikini, mahusiano huvunjika na mwisho watu kuchanganyikiwa na hivyo basi, nchi kuendelea kuwa masikini.

Mheshimiwa Spika, haya magonjwa yasiyo ya kuambikiza ni ghali kwa sababu magonjwa mengi matibabu yake ni ya maisha. Yaani mtu akishagunduliwa kwamba ana matatizo ya akili itachukua muda kumtibu huyu mtu mpaka apone kabisa. Mtu akigundulika ana magonjwa ya kisukari, mtu akigundulika ana shinikizo la damu, matibabu yake ni ya maisha, lazima awe anakwenda katika vituo vya afya mara kwa mara. Pia dawa za kutibu haya magonjwa ni ghali sana na hivyo huigharimu Serikali pesa nyingi kuyatibu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, visababishi vya magonjwa haya ni maisha ya kawaida ikiwepo na kutumia vitu kama tumbaku, pombe za kuzidi kiasi, vitu kama lishe isiyozingatia misingi ya afya, kwa mfano, kutumia sukari nyingi, mafuta mengi au chumvi nyingi. Vilevile kutoshughulisha mwili, kwa mfano kutokufanya kazi za kutumia misuli na vile vile kutokufanya mazoezi. Kuna sababu nyingine kwa mfano za uzee au za kurithi zinazosababisha magonjwa yasiyo ya kuambukiza, lakini haya hatuwezi kuyazuia.

Mheshimiwa Spika, ni vyema sasa Serikali ikatilia mkazo masuala ya magonjwa yasiyo ya kuambikiza. Moja katika sera yetu ni kutoa elimu. Hivyo basi, naishauri Serikali itilie mkazo elimu ya afya ya jamii katika jamii yetu ili tuweze kuzuia magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza ili wananchi wetu waweze kubaki salama. Naishauri Serikali kuimarisha kitengo hiki cha afya ya jamii katika Wizara. Hii itapunguza magonjwa mengi na hivyo kuipunguzia Serikali gharama kubwa ya kutibu magonjwa haya yasiyoambukiza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, itabidi sasa Serikali chini ya Waziri wetu mwenye dhamana ya afya kuangalia ni jinsi gani anaweza akatumia mbinu, interventions, katika kuhakikisha kwamba afya ya jamii inaenda mpaka ngazi za chini kabisa katika family level ili kuweza kugundua magonjwa haya na kuweza kuwaelimisha hawa wananchi kujua ni njia gani au ni visababishi gani vya magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya akili. Hivyo basi, naishauri Serikali kuimarisha kitengo badala ya kuimarisha zaidi tiba, iweze kuweka balance kati ya tiba na kuzuia. Pawepo na uwiano ulio sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata kama pesa nyingi zitawekezwa kwenye tiba, dawa na MSD, lakini vilevile katika kuzuia, pawe na uzito ule ule. Vijijini, wataalm wasambazwe huko; shuleni kuanzia msingi watoto wafundishwe kuhusu magonjwa yasiyo ya kuambukiuza ili watakapofika miaka 30 wajue wanafanyaje? Wajue kufanya mazoezi, wajue kula lishe bora ili hizo ndoa ambazo zimeshasemwa na wachangiaji ziimarike. Lishe bora iwekwe katika familia, watu wajue wanafanyaje katika kuzuia ili wasipate kisukari? Wanafanyaje kuzuia wasipate pressure? Wafanyaje ili wazuie kutokupata magonjwa ya akili kama yalivyosemwa na kushangiliwa hapa?

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, katika mchango wangu niseme tu, kinga ni bora kuliko tiba. Hilo halipingiki. Tuhakikishe kwamba sasa Wizara iweke kipaumbele pia katika kinga. Simaanishi kwamba tiba isiwepo, kwa wale ambao tayari wameshapata magonjwa haya, tiba iwepo, lakini tuzuie mafuriko kabla hayajaingia yatudhuru zaidi. Tuwekeze zaidi katika kinga. Sawa, haitachukua muda mfupi kama tunavyofikiria, lakini tuzuie ili ile generation inayokuja juu isiweze kupatwa na magonjwa hayo. Hata kama ikipatwa, basi iweze kujua namna ya kuishi nayo na namna ya kujua dalili za awali kabisa na kupata tiba mapema.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nami pia naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi nami nichangie katika Wizara hii ya TAMISEMI. Awali ya yote, napenda kumpongeza sana Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa juhudi zake nyingi sana na kubwa alizozifanya katika kuweka miundombinu mingi ndani ya miaka miwili katika sekta mbalimbali na hususan katika sekta ya afya na elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kuwapongeza Waziri pamoja na Manaibu Waziri wa TAMISEMI kwa kazi nzuri wanazofanya, wamekuwa wasikivu, wamekuwa wakipokea simu kwa wakati, wamekuwa wakitoa ushauri na ushirikiano uliotukuka. Nawapongeza sana. Naomba nielekeze mchango wangu katika sehemu mbili; sehemu ya kwanza ni sehemu ya afya pamoja na elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunamshukuru sana Rais wetu kwa miundombinu mizuri katika sekta ya afya hususani majengo ya zahanati, hospitali na vituo vyote vya afya katika nchi yetu. Hiyo inaonesha dhahiri kwamba nia ya Rais kuwafanya Watanzania kuwa na afya, ni kubwa sana. Ni dhahiri kabisa kwamba wananchi wanapokuwa na afya, basi wanaweza kufanya shughuli zao za kuleta maendeleo. Kwa hilo nampongeza Rais sana kwa dhati pamoja na Mawaziri wanaohusika kwa kuliangalia hilo na kwa kulishughulikia kwa uangalifu na umakini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kila mafanikio kuna changamoto ambazo ni vizuri sisi Wabunge tukatoa ushauri ili tuweze kufikia mafanikio makubwa zaidi ya hapa ambapo tumefikia. Ni imani yangu kabisa kwamba Mawaziri watayachukua na yatafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la ajira katika masuala ya afya. Ajira ni changamoto, hospitali zipo na wagonjwa wapo kila siku, lakini wafanyakazi ni wachache. Tukiangalia katika hospitali zetu nyingi kutokea zahanati mpaka hospitali kubwa, Madaktari hawatoshi, ni wachache; Manesi ni wachache; na Wataalamu wa Vifaa vinavyotumika hospitalini ni wachache au hawapo, wale ambao wanaweza kutunza vifaa na wale ambao wanaweza kufanya matengenezo pale ambapo vifaa vinaharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ushauri wangu, nilikuwa naomba tu, katika suala hili la ajira, kwa kweli kada ya hawa watu ambao ni Madaktari, Manesi, Wataalam, Wafamasia na wengine wa Maabara kwa kweli waajiriwe kwa wingi ili wananchi wanapoenda hospitalini, hii isiwe ni changamoto kwao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba pia kuishauri Wizara kuangalia vifaa mbalimbali vinavyotumika katika hospitali. Kuna vifaa kwa mfano hematology machines, hizi ni chache, hebu Wizara iweze kuziangalia na kuziongeza. Kuna chemistry analyzers, kuna mashine za theater kama Anesthesia Machines, ventilators, na mashine nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi mashine wananchi wanazitumia, na wanapozikosa katika maeneo yao na wanapopewa referrals kwenda katika hospitali kubwa, inakuwa ni changamoto kwa sababu wananchi wengi hata uwezo wa kupata nauli hakuna. Kwa hiyo, naomba TAMISEMI iweze pia kuzingatia hivyo vifaa viweze kupatikana katika hizo hospitali na zahanati ambazo zimejengwa katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda pia kulishauri katika Wizara ya Afya ni eneo la mafunzo kazini. Manesi wengi wana umri mkubwa, wamesoma zamani, kwa hiyo, wakipata na nafasi ya kwenda kuhudhuria mafunzo yatawasaidia kwa sababu teknolojia inabadilika mara kwa mara, hata vitu mbalimbali vinabadilika. Kwa hiyo, naishauri Wizara iweze kutenga pesa ya watumishi kwenda kupata refresher courses ili waweze kuwa updated pamoja na mambo yanavyokwenda na magonjwa yanayoibuka mara kwa mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda, naomba nigusie kwa haraka sana katika suala la elimu. Katika suala la Elimu ni dhahiri kabisa ya kwamba hata ukiwaweka wanafunzi katika hoteli ya five stars, kama wafanyakazi hawapo, kama walimu hawapo, watakaa, watakula na watapata kila kitu, lakini mwisho wa siku kama hawajafundishwa, ukiwa compare na wale ambao wamejifunza chini ya miti lakini walimu wapo, ni ukweli kabisa kwamba wale wa chini ya miti watafanya vizuri kuliko wale wanaokaa katika five stars hotel. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema nini? Namshukuru sana Rais kwa kujenga madarasa, kwa kujenga miundombinu, lakini waongezeke ili kuwe na balance ya wanafunzi wetu kufurahia mazingira na kufurahia walimu ili waweze kufaulu kwa kiwango kinachohitajika katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine pia niweze kushauri juu ya miundombinu ya walemavu katika shule zetu. Walemavu wanapata shida hasa katika miundombinu kama vile choo. Kwa hiyo, naomba pale tunapoendelea kufanya kazi yetu vizuri, tuzingatie vyoo hasa kwa wale ambao wana ulemavu wa viungo. Vile vyoo kwa kweli usafi wake kuu- maintain ni ngumu. Kwa hiyo, at least wawe na vyoo vyao special ili nao waweze ku-enjoy fursa kama wanafunzi wengine ambao hawana ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba kusema jambo moja kuhusu uzio. Naomba Serikali iweze kufikiria kujenga uzio katika shule zetu ili wanafunzi wetu waepuke vishawishi katika shule hasa wanapokuwa shuleni. Ule uzio utaweza kusaidia wasiweze kupata vishawishi nje ya maeneo ya shule. Wanapokuwa shuleni waweze kuzingatia kusoma tu na uzio japo hautamaliza, lakini utawazuia kutokutoka nje na kukutana na watu ambao nia zao siyo nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii. Nami naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi nami nichangie katika Wizara hii ya Afya. Awali ya yote, napenda kumshukuru Mungu kwa kunijalia afya na kusimama leo na kuweza kuchangia katika Wizara.

Mheshimiwa Spika, pia naomba kumshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kujali afya ya wananchi wote na hivyo kuipatia Serikali fedha nyingi sana ili huduma ya afya iweze kuboreshwa kuanzia katika ngazi ya vijiji mpaka ngazi ya juu. Napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Waziri na kumshukuru sana Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa kazi nzuri anayoifanya. Kwa kweli ni mchapakazi, pamoja na Naibu wake, timu yote na Madaktari wote Tanzania kwa kazi nzuri wanayoifanya. Nawapongezeni sana, kwani hii kazi ni nzuri, ni kazi ambayo ni ya muhimu kwa sababu bila afya kwa wananchi, maendeleo hayawezi kupatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimeipitia hii bajeti na kwa kweli inatia moyo sana, na kwa kweli tumepiga hatua na tunaenda sehemu nzuri. Naomba nichangie kwanza kwa kuipongeza sana Wizara ya Afya kwa mambo matatu ambayo wameyaleta na wanakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo la kwanza, nawapongeza kwa kuja na mpango wa uzalishaji, uratibu na kuwatumia wahudumu wa afya katika ngazi ya jamii (Integrated and Coordinated Community Health Workers Programme). Hii ni muhimu sana, na kwa kweli italeta mafanikio makubwa sana katika Wizara ya Afya na afya kwa ujumla. Kwa sababu katika ngazi ya familia ndipo walipo watu wengi, hawajulikani na hawaendi kupata matibabu wanapoumwa. Kwa hiyo, hii programu italeta mafanikio makubwa kwa sababu hao watakaokuwa trained watakuwa kule katika ngazi ya chini katika vijiji, na watakuwa wanawafahamu watu na tamaduni na hata lugha mbalimbali za watu, na hivyo hii programu itasaidia sana kupunguza gharama au mzigo mkubwa kwa Serikali katika kuleta tiba katika hospitali zetu kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa pika, kwa hiyo, kwa hilo naipongeza sana Wizara ya Afya kwa kuja na mpango huu. Nina hakika, hata nchi ya Rwanda ambayo Bunge liliwahi kunituma kuwakilisha, waliona hilo kwamba lilikuwa ni jambo lililokuwa na mafanikio. Naipongeza sana Wizara kwa kuliona hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, naipongeza sana Wizara kwa kuanzisha programu ya kuwa na Bachelor of Science Psychology katika Vyuo Vikuu nchini, kwa kuanzia na Chuo Kikuu cha MUHAS. Tatizo la afya ya akili limeongelewa mno na hata Mheshimiwa Ummy Mwalimu inaonekana sasa hivi anaijua vizuri hii changamoto ya afya ya akili. Afya ya akili ni chanzo cha matatizo ya magonjwa mengi. Hivyo basi, programu hii inapoanza itaenda kutoa suluhisho la matatizo mengi ya magonjwa ambayo yanaambatana na magonjwa ya akili. Kwa hiyo, naipongeza Serikali.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, naipongeza Serikali kwa kuipandisha hadhi Hospitali ya Mirembe kutoka katika jina hili na kuifanya kuwa Taasisi ya Taifa ya Afya ya Akili. Hili jina “Mirembe” kwa kweli lilikuwa linaleta unyanyapaa (stigma). Neno “Mirembe” hata mtu wa kawaida akiambiwa, anaonekana kama ni kichaa. Kwa hiyo, sasa hivi Wizara kwa kuliona hilo, na kubadilisha hospitali hii na kuipa hadhi, itaonekana ni seheme ya kawaida kabisa kama hospitali nyingine zozote nchini. Kwa hili nawapongeza sana, sana, sana Wizara ya Afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie mambo manne kwa Wizara yetu ya Afya. Jambo la kwanza, niwaombe kama nilivyowahi kuchangia, kuwekeza zaidi kwenye kuzuia magonjwa yasiyo ya kuambukiza (Non-Communicable Diseases). Naomba sana hili suala tuliangalie. Magonjwa mengi ambayo siyo ya kuambukiza, yanaleta changamoto. Gharama za kutibu magonjwa haya ni ghali na kwa kweli yana-consume fedha nyingi sana. Kwa hiyo, kama tutawekeza uzito katika kuzuia magonjwa haya yasiyo ya kuambukiza, hakika mambo yatakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, ninaishauri Serikali au Wizara kupanua wigo wa huduma ya vipimo (Diagnostic Services) katika jamii zetu. Kwa sababu kuna magonjwa mengi ambapo yanapogunduliwa mapema, kwa mfano kansa, inatibika, lakini mara nyingi wagonjwa wanakuja hospitali wakiwa tayari wako katika stage nyingine. Kwa hiyo, tuboreshe pia hizi huduma za kugundua magonjwa yanapokuwa katika stage ya awali kabisa.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, naomba kuishauri Serikali, kutokana na mabadiliko ya mara kwa mara ya teknolojia ya afya, Wizara itenge fedha kwa ajili ya elimu endelevu kwa watumishi wa Wizara ya Afya. Mambo yanabadilika kila siku, kwa hiyo, in service training, workshop pamoja na kozi fupi fupi kwa wafanyakazi wa afya au watoa huduma wa afya itawasaidia kuwafanya watoe huduma iliyo bora zaidi, inayoendana na teknolojia na mabadiliko yanayotokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la nne, naendelea kuishauri Serikali kwa kutoa motisha kwa wafanyakazi wanaofanya kazi vijijini. Watoa huduma wa afya wanapopelekwa vijijini wanaanza kufikiria maisha ya kijijini, kwa hiyo, wanakata tamaa, wanatamani kupangwa mijini. Naiomba Serikali tu iweze kutoa motisha; itoe incentives ili daktari au mtoa huduma anapopelekwa kijijini afurahie, ajue kwamba mimi kumbe kule kijijini nitakuwa aidha tofauti na wa mjini au nitakuwa bora. Kwa hiyo, atafurahia kwenda kufanya kazi vijijini, kuliko hivi sasa ambapo anayekwenda kijijini akifikiria kupata nyumba, akifikiria hali ya kijijini, anaanza kujifikiria mara mbili mbili, anatamani kufanya kila mbinu ili abaki mjini. Watakapopata motisha, labda wao na familia zao, na uhakika pengine wa kupata malipo ya ziada kwa kazi wanayofanya vijijini, kwa sababu tunajua vijijini changamoto ni nyingi. Kwa kweli wafanyakazi wengi watatamani kwenda vijijini hata kuliko kubaki mijini kwa sababu wanajua wataangaliwa kwa jicho tofauti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ajili ya muda, naomba kuipongeza tena Serikali kwa kazi nzuri. Naomba kuwashukuru sana Wizara kwa kuiangalia hili.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia katika Wizara hii. Napenda kumshukuru Mungu kwa kunipa afya njema tena kusimama na kuchangia katika Wizara hii muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia napenda kumshukuru Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa mara nyingine tena kwa kuona umuhimu wa kuwa na Wizara hii muhimu ambayo itashughulika na masuala ya maendeleo ya jamii yetu. Napenda kuwapongeza sana Mawaziri, Dkt. Gwajima pamoja na Naibu Waziri na watendaji wote pamoja na wafanyakazi wote wanaofanya katika Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii.

Mheshimiwa Spika, leo naomba kuchangia katika jambo moja linalohusu wajane. Katika takwimu hapa duniani kuonesha kwamba, kuna wajane takribani milioni 259 na nusu ya wajane haw ani maskini na huishi katika mazingira ya unyanyapaa, ubaguzi sababu ya jinsia zao pamoja na umri.

Mheshimiwa Spika, katika nchi zinazoendelea, hususan Tanzania, wajane wengi wanapopoteza wenza wao huchanganyikiwa kwa sababu, wajane wengi wanapoishi na wenza wao hushirikiana katika mambo mbalimbali ya kimahusiano, ya kiuchumi na kadhalika. Kwa hiyo, kifo kinapotokea, hasa kwa mwanaume, wajane hulia mara mbili, hulia kwa kupoteza wenza wao, lakini hulia muda mrefu kwa kufikiria maisha baada ya kupoteza wenza wao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wajane wengi katika Nchi ya Tanzania wanapofiwa na waume zao, tafiti zinaonesha kwamba, hupoteza hadhi zao kwa sababu, katika jamii yetu, wanawake huonekana kama ni wenza wasaidizi. Kwa hiyo, pale anapoondoka mwanaume, basi wao hujiona au huoenakana kwamba, hadhi kidogo imepungua, hata utu pia huonekana umepungua, lakini zaidi ya yote kipato hupungua baada ya kufiwa kwa sababu katika jamii zetu wanaume wengi ndio ambao huleta kipato katika familia. Vile vile wajane hupelekwa mbali, huenguliwa kwenye mambo ya urithi wa mali za familia na katika baadhi ya jamii zetu wanawake hurithiwa kutokana na ile mila iliyoko katika jamii hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, wajane ni kundi muhimu sana ambalo Serikali na jamii kwa ujumla ni vyema tukawaangalia kwa jicho la tofauti kwa sababu, wajane hawa mwisho wa siku huishia kuchanganyikiwa. Ikumbukwe kwamba, wajane ndio wanaotunza familia, wanawake hawa ambao sasa ni wajane na wanaachwa na watoto ambao ni yatima. Yatima ni mtoto ambaye amepoteza aidha, mzazi mmoja au wazazi wote, kwa hiyo, ninapoongelea wajane nawaingiza na watoto yatima ambao hulelewa na hawa wajane na mwisho wa siku hawa wajane hushindwa kulea watoto na hushindwa kufanya shughuli zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wajane mara nyingi wanapopoteza wenza wao wanakwenda Mahakamani kwenda kudai baadhi ya haki, ikiwepo mali. Hivyo, wajane hupoteza muda mwingi sana Mahakamani, wajane hupoteza muda mwingi sana katika mabaraza ya kifamilia, mabaraza yale ya usuluhishi na kadhalika na hivyo huathirika kisaikolojia na kushindwa kutekeleza kikamilifu majukumu yao katika jamii.

Mheshimiwa Spika, naongea kwa hisia kali kwa sababu, wajane ni wengi na ni kundi ambalo kwa kweli, wanahitaji sasa ifike mahali Wizara iwaangalie na waweze kuwa na nguvu kama wagane. Walie jambo moja kwamba, wamepoteza wenza tu na sio kupoteza vitu vingine na walee watoto kama wagane wanavyolea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaiomba Wizara ya Maendeleo ya Jamii kuhusu hawa wajane, kwanza katika jamii yetu elimu ya kutosha itolewe kwa jamii kabla hata watu hawajawa ama wagane au wajane, kwamba kuwa mjane ni ile hali tu ya kupoteza mwenza na siyo kupoteza vitu vingine. Kwa sababu sasa hivi kuna vurugu nyingi ambapo wanawake wanajiandaa wanakuwa wakali na hivyo changamoto ni kubwa sana katika jamii zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hivyo basi, mimi naishauri tena Wizara hebu iunde kitengo maalum ambacho kitawaangalia wajane na kuwapa elimu ya kutosha ili waweze kuelewa haki zao na nini wafanye pale ambapo mtu atakuwa mjane kwa sababu kifo hakizuiliki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu, ninaomba Wizara iangalie kupata msaada wa kisheria jinsi ambavyo hao wajane wanapopata changamoto wanaweza kupata msaada wa kisheria wapi, sehemu gani waende ili waweze kupata msaada wa kisheria, pia waweze kupata msaada ili wasibaguliwe katika familia zao, vilevile wasipate ukatili wa aina yoyote.

Mheshimiwa Spika, naomba kuishauri Wizara sasa ifike mahali ambapo isomeshe wataalamu katika ngazi ya vijiji ambao watapata ujuzi wa kuwasaidia wajane kuzielewa haki zao, kuwafariji ili wasipate zile changamoto waweze kuendelea kulea familia zao, waweze kuchangia katika maendeleo ya jamii yetu na vilevile tusizalishe watoto ambao watakuwa wamechanganyikiwa au ambao watashindwa kusoma vizuri na mwisho wa siku hao watoto hubakia kuwa watoto wa mitaani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia, nami pia naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi na mimi nikachangie katika Wizara hii. Awali yayote napenda kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipatia nafasi na mimi kusimama mbele kuchangia katika Wizara hii muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kumshukuru sana Rais wetu mpendwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa maono aliyoyapata ya kuweza kuanzisha Wizara hiii. Wizara hii ni muhimu sana, Wizara hii ilipokuwa katika Wizara ya Afya ilikuwa ni kubwa mno kiasi kwamba akili yote au concentration yote ilikuwa katika masuala ya afya, lakini leo Wizara hii inajitegemea na mimi sina mashaka na Dkt. Gwajima pamoja na Naibu Waziri pamoja na timu nzima ni wachapakazi. Kwa hiyo, kwa hilo naipongeza sana wizara hii kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la ukatili wa kijinsia limeongelewa sana kwa hisia kali na suala hili la ukatili wa kijinsia huwanyima wanaume na wanawake na watoto kufurahia haki zao za msingi ambazo kimsingi ni haki ya binadamu.

Mheshimiwa Spika, katika takwimu za Benki ya Dunia ambayo ilitolewa Aprili, 2022 imeonesha kwamba Tanzania ina asimilia 40 ya wanawake wote wameathiriwa kimwili au kijinsia na ambapo kati ya hao asilimia 14 wameathiriwa kwa kingono.

Mheshimiwa Spika, takwimu hizo hizo za Benki ya Dunia zinaonesha kwamba wanakwake wa umri kati ya miaka 15 mpaka 49 walifanyiwa ukatili huo na wenzi wao. Takwimu inaendelea kusema kwamba kwa wastani asilimia 30 ya wasichana chini ya miaka 18 walifanyiwa ukatili wa kingono.

Mheshimiwa Spika, hili suala ni zito, ukatili wa kijinsia ni jambo zito, ni jambo zito kwa sababu haliathiri tu maumbile, linaathiri hisia za wote wanaoathirika na mtu akiathirika kisaikolojia na kihisia ni rahisi sana kufanya mambo ambayo hakuyapenda kuyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aina za ukatili ambazo zinafanyika katika nchi yetu mojawapo ni ukatili wa kimwili kwa mfano mtu kupigwa au kujeruhiwa, nyingine ni ukatili wa kingono ambapo mtu huingiliwa bila ridhaa yake, inaweza ikawa ndani ya ndoa au ikawa nje ya ndoa, lakini kama hakuna ridhaa basi pia huo ni ukatili wa kingono, lakini pia kuna ukatili wa kisaikolojia, ukatili wa kisaikolojia; ni pale ambapo mtu anaumizwa kihisia na kujisikia vibaya na kutokufurahia Maisha, lakini ukatili mwingine ni ukatili utokao na mila na desturi zilizopo katika jamii zetu hizo ni kwa mfano kutokumiliki ardhi na wengi waathirika ni wanawake na nyingine ni ukeketwaji wa wanawake, nyingine ni ndoa za kulazimishwa, nyingine ni wajane katika mila mbalimbali kurithiwa lakini nyingine ni mauaji ya vikongwe wasiokuwa na hatia kwasababu mbalimbali. Lakini vilevile ni uuaji wa watu wenye ulemavu na nyingine ambayo pia ni ya ajabu ni miiko ya vyakula, kwa mfano wanaume hula chakula cha aina fulani na wanawake hawaruhusiwi kwa mfano kuku mapaja na nini wanaume ndiyo wanakula huo pia ni unyanyasaji wa kijinsia lakini vilevile hata ndoa ya mkeka pia ni unyanyasaji wa kijinsia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala kubwa linaloonekana hapa pia ambalo linachangia ni tatizo lipo ndani ya familia; ndoa zinakufungwa lakini baada ya muda panakuwa hakuna mawasiliano, baba na mama hawaongei miezi sita, mwaka watoto itakuwaje? Na hawa watoto ndiyo sisi huenda humu ndani na sisi wazazi wetu walifanya hivyo au babu zetu walifanya hivyo, baba kivyake, mama kivyake, baba anampiga mama, watoto wanaona, baba anamtukana mama watoto wanaona, watoto wanatukana, watoto wanaona, watoto hawaweze kuwapiga wazazi, mwisho wa siku watoto wanaamua kuondoka nyumbani na kwenda kutafuta maisha sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lambo muhimu sana pia katika tafiti nyingi zimefanyika hata hawa wazazi hawajui jinsi ya kuongea na watoto wao. Hawajalelewa katika mazingira ya kuongea na watoto, hawajui waongee na watoto wapi, hawajui waongee na watoto lini, hawajui mbinu gani watumie kuongea na watoto. Watoto hawana uhuru na wazazi, watoto wamesema hawana uhuru ukiwauliza watoto wanasema ni afadhali akaongee na mwalimu na je, hata hawa walimu wameandalia. (Makofi)

Kwa hiyo hili jambo Wizara iliangalie, wazazi wapewe semina ya kutosha kuongea na watoto wao. Wazazi wanaishi na watoto wenyewe warekebishe tabia zao, lakini wawe karibu na watoto ili waongee nao. Watakapoongea na watoto watajua shida zao na mtoto atakuwa na furaha, hatokimbia nyumbani, hatoenda mitaani hata kama familia kiuchumi siyo nzuri mtoto atashiriki katika masuala ya uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kutokana na muda naomba niongee suala moja muhimu sana. Suala hili ni kuhusu hivi vituo vya kulelea watoto. Vituo viko vingi lakini naomba kuishauri Serikali, hivi vituo miongozo yake haieleweki watu wanakurupuka wanaanzisha vituo, miundombinu haijakaa vizuri, wataalam wa kutosha hawapo na hivyo unakuta wapo tu wanaanzisha vituo watoto wanalala chini, watoto mara wanakosa mlo, watoto wanapigana, watoto hivi, wataalam hakuna, na kadhalika. Hivi vituo viangaliwe, vigezo vya kutosha, checklist iwepo ili hivi vituo viwe vituo kweli vitakavyoleta watoto watakavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa ninaomba tu...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MHE. DKT. PAULINA D. NAHATO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)