Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Dr. Festo John Dugange (882 total)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa niaba ya wananchi wa Mafinga, nafarijika kwamba katika zile Halmashauri 19 za Miji, Mafinga nayo itakuwemo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na jibu la msingi, naomba Serikali iweze kuwaambia wananchi wa Mafinga, mazungumzo haya na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuanza kutekeleza program nyingine ya kuendeleza miundombinu katika hiyo Miji 26 na 18 yatakamilika lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hali ya barabara zetu wakati huu ambapo mvua sasa zimeanza kunyesha kwa wingi, maeneo mengi nchi nzima barabara zimekatika baina ya eneo moja na nyingine: Je, Serikali kupitia TARURA iko tayari kutenga fedha za emergence na fedha hizi zikakaa kule kule Wilayani kuliko ilivyo sasa ambapo Wilaya au Mji kama Mafinga inabidi tuombe Emergence Fundkutoka TARURA Makao Makuu; sasa when it is emergence, imaanishe kweli ni emergence: Je, Serikali iko tayari kutenga Emergence Fundkwa ajili ya barabara ambazo zimeleta matatizo wakati kama huu wa mvua nyingi?
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafingi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika,ni kweli kwamba mazungumzo kati ya Serikali na Benki ya Dunia kuhusu miradi hii ya kuendeleza Miji inaendelea. Niseme kwamba maongezi haya yanaendelea na tunaamini kwamba mipango iliyoko na mwelekeo wa haya mazungumzo haitachukua muda mrefu kukamilisha mazungumzo haya. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kwamba Serikali inakwenda kutekeleza suala hili kwa ufanisi iwezekanavyo mara baada ya mazungumzo haya kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili kuhusiana na miundombinu ya barabara na je, kama Serikali iko tayari kupeleka fedha za dharura kupitia TARURA katika Wilaya kwa ajili ya kuhudumia barabara zilizoharibika. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kupitia TARURA imejipanga ku-respondkwa wakati kutatua changamoto za miundombinu ambayo itatokana na uharibifu wa mvua ambazo zinaendelea kunyesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mara tu changamoto hizi zitakapoonekana katika maeneo husika, naomba nimhakikishie kwamba Serikali iko tayari na tutahakikisha tunatatua changamoto hizo kwa wakati. (Makofi)
MHE. DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, kaka yangu Dkt. Dugange kutoka Wanging’ombe, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jibu la msingi tumesema kwamba inatokana na mapato ya kipindi husika asilimia 10, napigia mstari neno kipindi husika. Naomba kupendekeza maboresho kwamba halmashauri zinapokusanya pesa, let say, ya 2020; baada ya yale marejesho, inapokwenda 2021, ichukuliwe ile ya 2020 ichanganywe na 2021, ule Mfuko uwe Cumulative Revolving Fund na fedha ziwe nyingi. Halafu tunapokwenda 2022 tunachanganya ile miaka miwili, yaani Mfuko unakuwa mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, je, hatuoni sasa wakati umefika wa kukusanya ule Mfuko wa kukopesha ukawa ni Revolving Fund?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, hatuoni kama wakati umefika, maafisa wanaosimamia mikopo hii wakapata elimu kama Maafisa Mikopo katika benki zetu ambao mara nyingi ni Maafisa Maendeleo ya Jamii kama Loan Officer?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mikopo ya asilimia 10 kutolewa kwa kipindi husika, kama ambavyo jibu la msingi limesema, ni kweli kipindi husika cha makusanyo ndicho ambacho tumesisitiza kama Serikali kuhakikisha halmashauri zinatenga asilimia 10 kwa ajili ya mikopo kwa makundi hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo hiyo ni ile ambayo inahusisha wajasiriamali ambao fedha zile ambazo zinakopeshwa zinatakiwa kurejeshwa ili kutoa fursa kwa vikundi vingine kuweza kukopa fedha hizo. Kwa hiyo, napokea ushauri mzuri wa Mheshimiwa Dkt. Pindi Chana kwamba tutaendelea kusimamia, kuhakikisha kwamba mapato yanayokusanywa kwa kipindi husika, asilimia 10 inatengwa na kupelekwa kwenye vikundi hivyo ili kuwawezesha kuendesha shughuli zao za ujasiriamali kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana naMfuko huu kuwa Revolving Fund, kimsingi Mfuko huu ni Revolving Fund mpaka sasa, kwa sababu baada ya kukopeshwa, vikundi vinarejesha kiasi cha fedha kilichokopwa bila riba kwa ajili ya kuwawezesha wakopaji wengine waweze kunufaika na mfuko huo. Kwa hiyo, tutaendelea kuelimisha jamii yetu na vikundi vya wajasiriamali kuweza kurejesha mikopo hiyo ili na wengine wapate fursa hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na mchango na ushauri wa kuwa na maofisa ambao wanapata mafunzo mbalimbali ya mifumo hii katika benki na maeneo mengine, tunauchukua ushauri huo.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika mimi nasikitika sana, kata hii ina vijiji 16 hakuna mawasiliano kati ya kijiji hiki na kijiji kingine. Madaraja yote yamekwenda na maji, mito na barabara zote zimeunganika. Wananchi wa Kata ya Katumba wanapata shida sana. Je, ni lini Serikali itatengeneza barabara za wananchi wa Kata ya Katumba? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, Naibu Waziri yuko tayari kwenda na mimi tukimaliza tu Bunge tukatembelee Kata ya Katumba yenye vijiji 16 ili aone uhalisia wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna changamoto ya barabara katika Halmashauri ya Nsimbo na katika kata hii husika, lakini Serikali katika bajeti ya Wilaya ya Nsimbo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 ya shilingi milioni
556 tayari shilingi milioni 148 sawa na asilimia 27 zimekwishapelekwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kwa ajili ya kutekeleza miundombinu ya barabara ambazo zinaunganisha vijiji husika.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwanza Serikali inatambua changamoto hiyo na ndio maana imepeleka fedha kiasi hiki kwa ajili ya ukarabati wa barabara hizo na madaraja hayo na nimhakikishie kwamba utaratibu wa kuendelea kupeleka fedha nyingine kwa ajili ya kuimarisha miundombinu katika Halmashauri ya Nsimbo na katika vijiji hivi vya kata hiyo unakwenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba, niko tayari baada ya shughuli za Bunge kwenda naye katika Halmashauri hiyo kupitia vijiji hivyo ambavyo vinahitaji matengenezo ili tuweze kuongeza nguvu pamoja na kuondoa changamoto za wananchi. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama lilivyo swali la msingi, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwenye Wilaya ya Kyerwa tuna kata 24 lakini tuna vituo vya afya vitatu; Serikali ina mpango gani wa kuongeza vituo vya afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Kituo cha Afya Nkwenda ni kituo ambacho tumeanzisha jengo la mama na mtoto ambalo bado halijakamilishwa. Serikali ina mpango gani wa kukamilisha Kituo cha Afya Nkwenda kwenye jengo la mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Halmashauri ya Kyerwa kuwa na kata 24 na vituo vya afya vitatu tu na Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba halmashauri hiyo inapata vituo vya afya kadri ya maelekezo na sera. Kama ambavyo nimetangulia kusema kwenye jibu la msingi, Serikali imedhamiria kuhakikisha inasogeza huduma za afya karibu na wananchi kwa kuunga mkono ujenzi wa vituo vya afya katika kata.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa utekelezaji wa miradi hii ya ujenzi wa vituo vya afya katika kata ni endelevu na ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha tumetenga shilingi bilioni 27.75 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vituo 555. Pia katika mwaka wa fedha ujao tutatenga bajeti kwa ajili ya kuendelea kujenga vituo hivyo. Halmashauri ya Kyerwa na kata zake ni sehemu ya halmashauri na kata ambazo zitanufaika katika mradi huu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili litafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kituo cha afya kuwa na jengo la wazazi na Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha jengo hilo linakamilika na kutoa huduma. Hilo ni jambo la muhimu sana katika kusogeza huduma kwa wananchi. Kwa sababu Serikali inatambua na ina dhamira ya dhati ya kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga, kipaumbele ni pamoja na kutenga fedha kadri zinavyopatikana kwa ajili ya kukamilisha majengo kama haya. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba pia jengo hilo litakuwa sehemu ya mpango huu ili liweze kukamilishwa na kutoa huduma zinazokusudiwa kwa wananchi.
MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kijiji cha Migungumalo, Kata ya Usagari, Marehemu Mheshimiwa Benjamin William Mkapa alizindua zahanati ndogo na aliahidi kwamba pale patajengwa kituo cha afya ili iwe hospitali kubwa ambayo atakuja kuifungua tena. Nilipoingia madarakani tumeanzisha kujenga kituo kile na kwa uchungu sana nilikuwa nimepanga kwenda kumwambia Mheshimiwa Benjamin Mkapa kwamba sasa ajiandae kuja kufungua kituo kile na bahati mbaya Mheshimiwa Mkapa amefariki, Mungu aiweke roho yake mahali pema peponi. Nimeshamwambia Mheshimiwa Rais juu ya suala hilo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Maige, swali lako la nyongeza?

MHE. ALMAS A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu, kwa vile kituo kile tunakijenga kwa nguvu za wananchi, je, Serikali ina mpango gani wa kukimalizia kituo hicho ili heshima ya Marehemu Benjamin Mkapa ihimidiwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Tabora Kaskazini kwa kuchangia maendeleo na kuanza ujenzi wa kituo hicho cha afya ambacho lengo ni kupandisha hadhi ya zahanati kuwa kituo cha afya. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Maige kwamba katika bajeti ya Serikali ya kwenda kukamilisha majengo ya zahanati na vituo vya afya ambayo imetengwa katika mwaka huu wa fedha katika halmashauri yake na katika jimbo lake, jumla ya vituo vinne vimetengwa na jumla ya shilingi milioni 200 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo eneo hilo la kituo hicho cha afya ambacho ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, basi tutakwenda pia kuona namna gani tunashirikiana katika bajeti hii, lakini pia katika bajeti zinazofuata, ili tuweze kukikamilisha kiweze kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyokusudiwa.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo la vituo vya afya vilivyopo kwenye Jimbo la Tabora Kaskazini ni sawa na lililopo kwenye Jimbo la Igunga, Kata za Isakamaliwa, Kining’inila na Mtungulu. Ni kata ambazo hazina vituo vya afya vya kata na sisi kama wananchi tumeanza kutoa nguvu yetu kusaidia wananchi kujenga vituo vya kata. Je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi kukamilisha vituo vya hizo kata husika ili tuweze kuwapatia wananchi huduma ya afya? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuunga mkono nguvu za wananchi katika ujenzi wa vituo vya afya katika kata. Katika bajeti ambayo imetengwa lengo ni kuhakikisha kwamba kadri ya upatikanaji wa fedha nguvu za wananchi zitaendelea kuungwa mkono kwa Serikali kupeleka fedha ili kukamilisha vituo vya afya na zahanati zinazojengwa katika maeneo hayo. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Igunga kwamba Igunga ni sehemu ya halmashauri na kata zake ni sehemu ya kata nchini kote ambazo zitanufaika na mpango huu wa umaliziaji na ujenzi wa vituo vya afya ili viweze kutoa huduma kwa wananchi.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, tunajua kwamba Serikali ilisitisha uongezaji wa maeneo ya utawala lakini Serikali ilitoa ahadi hapa Bungeni kwamba yale maeneo ambayo hayatakuwa na gharama za uanzishwaji wake na hasa maeneo ya kata, kwa sababu kata zetu hizi ni kubwa mno katika baadahi ya maeneo. Je, Serikali itaanza kutekeleza ahadi hii lini ili kusogeza huduma karibu na wananchi wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, barabara hizi ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri amezizungumzia hapa zimekuwa zikiharibika mara kwa mara na hasa wakati huu wa kipindi cha mvua. Uwezo wa TARURA kuendelea kuzikarabati hizi barabara unaonekana unapungua siku hadi siku kwa sababu ya mgao mdogo ambao wanaupata kutoka kwenye fedha za Bodi ya Barabara. Je, Serikali haioni umefika wakati sasa wa kuanzisha chanzo maalum cha fedha kupelekwa kwenye TARURA badala ya kutegemea hisani kutoka kwenye Mfuko wa Barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, Mbunge wa Mtama, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali ina mpango na dhamira ya dhati ya kusogeza huduma za jamii karibu na wananchi kwa kuanzisha maeneo ya utawala ambayo hayatakuwa na gharama kubwa. Kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema, naomba nimhakikishie kwamba dhamira hiyo ya Serikali ipo na utaratibu wa kuomba maeneo hayo unafahamika na nishauri kwamba pale ambapo tunaona kuna kila sababu ya kuanzisha maeneo hayo yanayofuata maelekezo ya Serikali ya kuzingatia kutokuongeza gharama, basi maombi yawasilishwe kwa mujibu wa taratibu Ofisi ya Rais TAMISEMI ili yaweze kufanyiwa kazi kwa kadri ya taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la nyongeza la pili la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye ni kuhusiana na barabara zinazohudumiwa na TARURA. Ni kweli Wakala wa Barabara Vijijini na Mjini ina jukumu kubwa la kuhakikisha miundombinu ya barabara inapitika mwaka mzima. Wakala huyu ana mtandao wa barabara zipatazo kilometa 108,496 ambazo hufanyiwa matengenezo mara kwa mara na pale inapobidi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba bado bajeti ya TARURA haitoshelezi lakini Serikali imekuwa ikiongeza fedha mwaka hadi mwaka ili angalau kuendelea kuboresha utekelezaji wa wakala huyu. Kwa mfano, kwa mwaka wa fedha 2019/2020, bajeti ya TARURA ilikuwa shilingi bilioni 241, lakini kwa mwaka 2020/2021 bajeti ya TARURA ni shilingi bilioni 275 ikiwa ni ongezeko la takribani shilingi bilioni 34. Ni kweli Serikali inaona sababu ya kutafuta vyanzo vingine vya kuongezea uwezo TARURA ili iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi mkubwa zaidi na jambo hili linaendelea kufanyiwa kazi.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba na mimi niulize swali moja la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Sengerema ina halmashauri mbili, Halmashauri ya Sengerema na Halmashauri ya Buchosa. Mimi ni Mbunge wa Buchosa, wakati wa kampeni nilimuomba Mheshimiwa Rais Halmashauri ya Buchosa nayo iwe Wilaya. Kwa hiyo, naomba kujua ni lini sasa Buchosa nao watakumbukwa kuwa Wilaya? Halmashauri hii ina mapato makubwa, ni halmashauri inayojitosheleza na inafaa kabisa kuwa wilaya ili huduma ziweze kuwasogelea wananchi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Erick Shigongo, Mbunge wa Buchosa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunahitaji kusogeza huduma za jamii karibu zaidi na wananchi na kuanzisha maeneo mapya ya utalawa. Ni sehemu ya kusogeza huduma kwa jamii.

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Buchosa ambayo Mheshimiwa Shigongo anaielezea, naomba nimshauri kwamba utaratibu wa kuomba maeneo mapya ya utawala unafahamika na Ofisi ya Rais, TAMISEMI bado haijapata taarifa rasmi kutoka Mkoa wa Mwanza, ukihitaji kuomba Halmashauri ya Buchosa kuwa Wilaya. Kwa hiyo, naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge, wafuate utaratibu huo na Serikali itaona namna gani ya kulifanyia kazi suala hili. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana lakini kwenye tablets zetu hatuna Order Paper.

Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, kumekuwa na utamaduni wa fedha nyingi zilizopangwa kwa ajili ya utekelezaji miradi mbalimbali ya barabara kucheleweshwa hivyo ufanisi wa kile kinachokusudiwa hakifikiwi. Je, Serikali sasa mko tayari kuhakikisha kama fedha zinatengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara yoyote zinatoka kwa wakati ili barabara hizo zitengenezwe?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara ya Karatu inatoka Njia Panda – Mang’ola - Lalago ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu. Barabara hii imekuwa ikiahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami hasa kipindi cha uchaguzi ahadi inakuwa ni tamu kweli masikioni mwa wananchi lakini baada ya hapo barabara hiyo haijengwi kiwango cha lami. Serikali mtuambie ni lini kwa hakika barabara hiyo itajengwa kwa sababu Sera ya Wizara ya Ujenzi inasema kuunganisha barabara za Mikoa na Mikoa kwa kiwango cha Lami na barabara ile inaunganisha Mkoa wa Arusha na Mkoa wa Simiyu?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kuhusu fedha za miradi mbalimbali ya barabara kuchelewa kupelekwa katika miradi hiyo, utaratibu wa fedha kupelekwa katika miradi mbalimbali unazingatia upatikanaji wa fedha ambazo zimetengwa kwenye bajeti husika. Hivyo, kutokana na kutegemea mapato ya ndani kupata fedha kwa ajili ya kutekeleza miradi hiyo, mara nyingi kumekuwa na ucheleweshwaji na miradi hiyo kwa sababu ya upatikanaji wa fedha. Hata hivyo, Serikali imeendelea kuongeza jitihada kuhakikisha kwamba mapato yanakusanywa kwa wakati na fedha za miradi hiyo zinawasilishwa kwenye miradi husika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa kipindi cha mwaka huu wa fedha mpaka sasa takribani asilimia 48 ya fedha ya miradi ya barabara tayari imekwishawasilishwa katika mamlaka ya Serikali za Mitaa na kazi za utekelezaji wa miradi hiyo zinaendelea. Suala hili litaendelea kufanyiwa kazi kwa karibu zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na barabara ya Arusha Simiyu inayotokea Karatu, ni kweli hii ni barabara muhimu sana na inaunganisha mikoa hii miwili. Serikali ina dhamira ya dhati kuhakikisha kwamba barabara hizi kuu ambazo zinaunganisha mikoa zinajengwa kwa kiwango cha lami ili kurahisisha shughuli za kiuchumi na za kijamii.

Mheshimiwa Spika, kama alivyouliza kwamba Serikali imekuwa ikitoa ahadi, ni kweli na ahadi ya Serikali hakika itatekelezwa. Nimhakikishie tu kwamba mara fedha zikipatikana barabara hiyo itajengwa ili wananchi waweze kupata huduma zilizokusudiwa.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwanza kabisa, napenda kuipongeza Serikali kwa jitihada kubwa za kuboresha miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Spika, napenda kumfahamisha Mheshimiwa Conchesta kwamba tayari kazi ya kuboresha barabara ile inaendelea ili iweze kupitika ambapo sasa hivi wanafanya kazi za kuchepua maji, kuweka mawe na changarawe. Vilevile napenda kumfahamisha Conchesta kwamba mimi pamoja na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Bukoba Vijijini tumeshawasiliana na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na barabara hii itafanyiwa kazi kwa kuzingatia mpango kazi uliowasilishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha, kwa kuwa umuhimu wa kipande hicho cha barabara unafanana na barabara ya Kanazi - Kyaka kupitia Katoro, ni lini barabara hiyo nayo itatengewa fedha na kujengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Lugangira, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Serikali ni kuboresha miundombinu ya barabara ikiwepo barabara hii ya Kanazi, Kyaka kupitia Katoro. Kimsingi tathmini na upatikanaji wa fedha kwa ajili ya kujenga barabara hizi unaendelea. Mpango umeandaliwa kwa ajili ya kufanya tathmini lakini kuhakikisha kwamba barabara hizi zinatafutiwa fedha ili ziweze kujengwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kutekeleza mipango yake hii ya kufanya tathmini lakini pia kutafuta fedha ili barabara hizi ziwezwe kujengwa na kusogeza huduma kwa wananchi.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali japo siridhiki nayo kwa sababu maeneo ya kujenga Hospitali ya Wilaya katika Jimbo la Mbinga Vijijini yapo mengi katika maeneo tofauti tofauti, ni uamuzi tu wapi tujenge hospitali hiyo. Je, Serikali inawahakikishia nini wananchi wa Mbinga Vijijini katika bajeti ijayo ikiwa bajeti mbili tofauti zimepangwa na hizi fedha hazikupelekwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wananchi wa Mbinga Vijijini kwa kuunga mkono juhudi za Serikali wamejenga na kukamilisha zahanati sita; zingine zina miaka miwili toka zikamilike. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka wahudumu katika zahanati hizi ili zifunguliwe zianze kuwahudumia wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye swali la msingi, kigezo muhimu cha kupeleka fedha katika Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ambacho Serikali iliweka ilikuwa ni Halmashauri husika kuainisha eneo na kuwasilisha taarifa ya uwepo wa eneo husika ndipo fedha ziweze kupelekwa kwenye Halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mbinga Vijijini imekuwa na mivutano ya muda mrefu kuhusiana na wapi Makao Makuu ya Halmashauri iwepo. Januari hii wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu alipopita ndipo ilipata majibu ya kuwa na Makao Makuu ya Halmashauri yawepo. Kwa sababu hizo, hawakuwa na eneo rasmi ambalo liliwasilishwa Serikalini na ndiyo maana fedha haikupelekwa. Hata hivyo, kwa sasa, kama nilivyosema kwa sababu wamekwishawasilisha eneo ambalo limetengwa, katika shilingi bilioni 27 ambazo zimetengwa na Serikali, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba watapata fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mbinga Vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na zahanati sita ambazo zimekamilika na hazijaanza kutoa huduma kwa sababu ya upungufu wa watumishi, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Kapinga kwamba Serikali inathamini sana kuanza kutoa huduma kwa wananchi wa Mbinga Vijijini. Kwa sababu zahanati hizi zimekamilika tutakwenda kuona utaratibu mzuri kwanza kwa kutumia watumishi waliopo ndani ya halmashauri kufanya internal redistribution ya watumishi hao angalau kuanza huduma za afya. Katika kibali cha ajira kinachokuja Halmashauri ya Mbinga Vijijini tutawapa kipaumbele ili watumishi hao waweze kwenda kutoa huduma katika zahanati hizo.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo. Kwa kuwa na sisi watu wa Makete tuna changamoto ya hospitali ya wilaya toka mwaka 1982 kituo cha afya kilivyopandishwa hadhi kuwa hospitali ya wilaya, hadi sasa hatuna hospitali ya wilaya. Je, ni lini Hospitali ya Wilaya ya Makete itaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2020/2021, kiasi cha shilingi bilioni 27 kimetengwa kwa ajili ya kujenga hospitali za halmashauri zile ambazo ni chakavu, tutajenga hospitali za halmashauri mpya na Halmashauri ya Makete ni miongoni mwa halmashauri ambazo tutakwenda kutenga fedha na kuhakikisha kwamba ujenzi wa hospitali ya halmashauri unaanza.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza dogo, kwamba Jimbo la Ndanda lenye kata 16 lina Kituo cha Afya kimoja tu cha Chiwale. Hata hivyo wananchi wa Ndanda, Lukuledi, Panyani, Mihima pamoja na Chilolo walijitahidi kwa kutumia nguvu zao pamoja na nguvu ya Ofisi ya Mbunge kujenga maboma kwa ajili ya zahanati na mengine kituo cha afya. Nini kauli ya Serikali kuhusu kuwapokea wananchi mzigo huu wa kukamilisha maboma haya ili yaweze kutumika na kutoa huduma za afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitumie nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Jimbo la Ndanda kwa kujitolea nguvu zao na kuanza ujenzi wa zahanati na vituo vya afya na hiyo ni kauli ya Serikali ya kuhakikisha kwamba wananchi wanaibua miradi na Serikali inaunga nguvu miradi hiyo ya wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka huu wa Fedha 2020/2021, Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 27.75 ambazo zitakwenda kufanya kazi ya kuchangia nguvu za wananchi katika kukamilisha ujenzi wa maboma 555 nchini kote. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mwambe kwamba jimbo lake na vijiji na kata husika zipo katika mpango huu na Serikali itahakikisha inatoa mgao kwa ajili ya umaliziaji wa vituo hivyo ili viweze kutoa huduma kwa wananchi.
MHE. JOSEPH K. MHAGAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile swali la msingi linalohusu Mbinga Vijijini linafanana kwa kiasi kikubwa na tatizo la Madaba na kwa vile Madaba ilishatengewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya na kwa vile kwa miaka miwili mfululizo fedha hiyo haijatoka. Ni lini sasa Serikali itapeleka fedha Madaba ili ujenzi wa hospitali ya wilaya uanze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mhagama, Mbunge wa Madaba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imekuwa ikitenga fedha kila mwaka wa fedha kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za halmashauri.

Katika kipindi cha miaka mitano sote tumeona kazi kubwa iliyofanyika kwa kujenga hospitali za halmashauri zaidi ya 101 na katika mwaka huu wa fedha, kiasi cha shilingi bilioni 27 zimetengwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika vituo na hospitali za halmashauri ambazo zitajengwa Jimbo lake la Madaba pia litapewa kipaumbele.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Swali langu la nyongeza; ni lini sasa Serikali itatoa vifaa vya upimaji kwenye wilaya ya Mbogwe? Maana Wilaya ya Mbogwe inakua na ina watu wengi sana, lakini hatuna vipimo vya x-ray pamoja na vipimo vingine. Kwa hiyo wananchi wa Mbogwe wamekuwa wakipata taabu sana wanapopata ajali wale waendesha bodaboda na watu wengine; ni lini Serikali inawahakikishia wananchi wangu wa Mbogwe kwamba itapeleka hivyo vifaa vya upimaji.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya kwenda kuongeza nguvu za kununua vifaa tiba katika hospitali mpya 67 za halmashauri kote nchini.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Mbogwe ni moja ya hospitali ambazo zitanufaika na bajeti hii kwa kupata kiasi cha shilingi milioni 500 kadri ya fedha itakavyopatikana ili ziweze kununua vifaa tiba kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na pia kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, lakini nataka niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa daraja hili linaunganisha tarafa zaidi ya tatu kwa maana Tarafa ya Suba, Nyancha pamoja na Luo- imbo na ni muhimu sana kwenye uchumi wa muunganiko wa watu wanaoishi ndani ya tarafa hizi.

Je, Mheshimiwa Waziri haoni kuna umuhimu wa kuharakisha daraja hili kwa kuwa si tu linaharakisha uchumi, lakini pia ni sehemu ambayo wananchi wengi wamekuwa wakipoteza maisha wanapovuka kutoka upande mmoja kwenda upande wa pili?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri haoni sasa baada ya Bunge hili, kuna umuhimu sasa wa kuongozana mimi na yeye ili kwenda pamoja kule ndani ya jimbo kuona namna gani tunaweza tukatatua pamoja changamoto hii ili angalau wananchi hawa waweze kupata huduma hii kwa uharaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba daraja hilo ni muhimu sana kwa kuwa linaunganisha vijiji vingi na tarafa tatu katika Halmashauri ya Rorya na kiungo muhimu sana katika shughuli za kiuchumi na shughuli za kijamii katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoongea katika majibu yangu ya msingi kwamba Serikali inatambua sana umuhimu wa daraja hilo na ndiyo maana katika mwaka wa fedha ujao 2021/2022 Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kufanya tathmini na usanifu ili kutambua shughuli ambayo inahitaji kutekelezwa na gharama za daraja hilo ili kadri ya upatikanaji wa fedha daraja hilo liwezwe kujengwa na kutatua changamoto hizo kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kuambatana na Mheshimiwa Mbunge naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tuko tayari wakati wowote kufika kushirikiana naye Mheshimiwa Mbunge. Baada ya kikao hiki tutapanga tuone ratiba bora zaidi ya kwenda kupita eneo hilo na kuona namna gani tunakwenda kuwahudumia wananchi.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Matatizo yalioko katika Daraja la Rorya ni sawa kabisa na matatizo yaliyoko kwenye Jimbo la Geita Vijijini kwenye Daraja la Blengete, Kata ya Isilobutundwe na tumeshaandika maandiko mengi lakini hatujawahi kupata majibu. Je, Wizara au Waziri yuko tayari sasa baada ya Bunge hili kuongozana nami kwenda kuona ili aone umuhimu wa kutupatia pesa hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameelezea daraja katika eneo hilo ni muhimu sana katika shughuli za kiuchumi za wananchi, lakini pia kwa shughuli za kijamii. Niwapongeze sana akiwemo mwenyewe Mheshimiwa Musukuma kwa jitihada za kufuatilia daraja hilo liweze kujengwa ili wananchi waweze kupata huduma. Naomba nimhakikishie kwamba, kadri ya upatikanaji wa fedha Serikali itaendelea kulipa kipaumbele eneo hilo la daraja na litaanza ujenzi pale bajeti itakapotengwa na fedha itakapopatikana.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Naibu Spika, Ahsante Sana. Naomba nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali la nyongeza. Daraja lililopo Jimbo la Moshi Vijijini lilisombwa na maji mwaka mmoja uliopita na daraja hili ni muhimu, linaunganisha kata nne katika Jimbo la Moshi Vijijini. Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa daraja hili? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua maeneo yote korofi ambayo madaraja yetu kwa namna moja ama nyingine yameathirika na mafuriko kutokana na mvua ambazo zimeendelea kunyesha hapa nchini. Serikali imeweka mkakati wa kwenda kufanya tathmini ya mahitaji katika maeneo hayo korofi ili kulingana na upatikanaji wa fedha, fedha ziweze kutengwa na madaraja hayo yaweze kujengwa au kufanyiwa marekebisho ili kuwezesha wananchi kupata huduma kama Serikali inavyodhamiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Moshi Vijijini kwamba eneo hilo Serikali inalitambua na tutakwenda kadri ya upatikanaji wa fedha kutenga bajeti kwa ajili ya usanifu, lakini pia kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo ili tuweze kurahisisha shughuli kwa wananchi.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali tayari Mheshimiwa Naibu Waziri amekiri kwamba halimashauri 85 hazijaweza kutekeleza kwa asilimia mia moja utoaji wa mikopo. Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuanzishwa kwa benki ya vijana ili iweze kusimamiwa na vijana wenyewe?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Serikali ina mpango gani juu ya kuwakopesha vijana mmoja mmoja kwa sababu vijana wengi wanaopewa mikopo hii haiendi kuwanufaisha kwa kuwa mawazo yanakuwa tofauti? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Asia Abdukarim Halamga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tumeona tangu kuanzishwa kwa mpango huu wa mikopo asilimia kumi kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kazi ya ukopeshaji katika ngazi ya halmashauri katika miaka mitatu iliyopita imeongezeka zaidi ya mara tatu. Kwa hivyo, kwa hatua hii bado Serikali inaendelea kutekeleza vizuri, lakini ni kweli kwamba bado kuna changamoto kwenye baadhi ya halmashauri kutokana na uwezo wa ukusanyaji wa mapato na ndiyo maana Serikali imeendelea kusisitiza halmashauri kuboresha vyanzo vya mapato.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na wazo la Mheshimiwa Mbunge kuanzisha benki ya vijana, naomba tulichukue kama Serikali, tukalifanyie tathmini na kuona njia bora zaidi ya kulitekeleza. Kuhusiana na mikopo ya vijana kwa maana kijana mmoja mmoja, pia ni wazo la Mheshimiwa Mbunge na sisi ni kazi yetu kuchukua mawazo ya Waheshimiwa Wabunge, kuyatathmini, kuyafanyia kazi na kuona uwezekano wa kutekeleza hilo. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inapokea mawazo hayo na tutakwenda kuyafanyia kazi na kuona njia bora zaidi ya kuyatekeleza.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nina swali moja la nyongeza; katika halmashauri zetu zipo SACCOS za vijana na wanawake ambazo zimeundwa na wanawake na vijana, lakini SACCOS hizo hazikopeshwi kupitia Mifuko ya Halmashauri. Sasa, ni lini Serikali italeta sheria Bungeni ili SACCOS hizo za vijana na wanawake ziweze kukopesheka kupitia Mfuko wa Halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika naomba kujibu mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika kuhusiana na SACCOS za vijana na wanawake kutokopesha kupitia halmashauri na wazo lake ni lini Serikali italeta sheria ili utaratibu huu uweze kutendeka, naomba nichukue wazo la Mheshimiwa Mbunge, tukalifanyie tathmini kama Serikali na kuona uwezekano wa kutekeleza jambo hili na kuona faida zake na changamoto zake ili tuweze kufanya maamuzi stahiki.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Halmashauri ya Jimbo la Kyerwa, tunalo jengo la halmashauri. Jengo hili limechukua muda mrefu na halijakamilishwa. Nini ahadi ya Serikali kukamilisha lile jengo la halmashauri katika Wilaya ya Kyerwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali ndiyo inayojenga majengo yote ya halmashauri katika nchi yetu likiwemo jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa. Hivyo basi, kutokana na mahitaji na malengo ya Serikali ambayo imejiwekea na bajeti ambayo tumeitenga, tutalikamilisha lile jengo kadri bajeti yetu tulivyoiweka. Ahsante sana.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa kuwa daraja hili linaunganisha Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Kilimanjaro na hivyo ku-facilitate kusafirisha mifugo pamoja na mazao ya kilimo kwenda mikoa mbalimbali kutoka mikoa ya Kati kwenda Kaskazini. Kwa kuwa kuwepo kwa daraja hili kutafupisha safari ya kutoka Kilimajaro kwenda Dodoma kwa kilometa 172. Kwa kuwa fedha zinazotengwa TARURA ni ndogo sana na haziwezi zikatosheleza ujenzi wa daraja hili kwa haraka. Je, Serikali, Wizara ya TAMISEMI, haioni kwamba umefika wakati sasa wa kushirikiana na TANROADS au Wizara ya Ujenzi kwa sababu imekuwa inafanya hivyo katika projects mbalimbali ili kuweza kunusuru wananchi katika maeneo mbalimbali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa wakati huu ni wakati wa amani na kwa kuwa Jeshi letu la Wananchi limekuwa linafanya kazi nzuri sana ya ujenzi wa miundombinu, je, katika madaraja haya ambayo yametajwa na Waheshimiwa Wabunge asubuhi ya leo pamoja na Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haioni kwamba inaweza kushirikisha Jeshi ili liweze kusaidia kujenga madaraja haya ili wananchi waweze kupita kwa urahisi na shughuli za uchumi zikaendelea vizuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Daraja hilo la Mto Pangani ni muhimu sana kwa sababu linaunganisha mikoa miwili; Mkoa wa Manyara na Mkoa wa Kilimanjaro. Ni kweli kwamba bajeti ya kawaida ya kuhudumia Halmashauri ya Same haiwezi kukamilisha ujenzi wa daraja hilo kubwa; na hivyo katika utaratibu wa Serikali kuna ujenzi wa taratibu za kawaida lakini pia kuna ujenzi maalum kwa maana ya kutenga bajeti maalum kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu korofi kama ilivyo daraja hilo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mbinu hizi mbili za matengenezo ya muda wa kawaida kwa maana ya utaratibu wa kawaida na matengenezo maalum hutumika pale ambapo madaraja yanahitaji fedha kiasi kikubwa kuliko bajeti ya halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili TARURA tumeendelea kushirikiana kwa karibu sana na TANROADS kuona namna bora ya kushirikiana ili daraja hilo liweze kupata suluhu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ushirikiano huu unaendelea vizuri na tunaamini kwamba katika mwaka wa fedha ujao tutakuwa tumefikia hatua nzuri ya utekelezaji wa ujenzi wa daraja hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la Jeshi kushiriki katika kujenga madaraja hayo, mara nyingi Serikali katika madaraja ambayo yanahitaji ujenzi wa dharura kutokana na maafa mbalimbali kama mafuriko, sote tumekuwa mashahidi kwamba majeshi yetu yamekuwa yanafika na kufanya matengenezo hayo kwa haraka na kwa wakati ili kurejesha huduma kwa wananchi. Jambo hili litaendelea kutekelezwa kadri ya matukio hayo hayavyojitokeza.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto zilizopo Same Magharibi zinafanana sana na changamoto zilizopo Jimbo la Busokelo. Kata ya Ntaba tuna Daraja ambalo linaitwa Mto Ngubwisya, liliondolewa na maji tangu tarehe 30 Aprili, 2019 na daraja hili linaunganisha Kata za Kisegese, Itete, Kambasegera pamoja na Luangwa.

Je, ni lini Serikali inakwenda kujenga daraja hili ili wananchi wangu wa Busokelo waunganishwe kama ilivyokuwa zamani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fredy Makibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba daraja hilo muhimu ambalo linaunganisha kata na vijiji mbalimbali katika Jimbo la Busokelo lilivunjwa na maji mwaka 2019. Serikali inatambua sana umuhimu wa kwenda kulifanyia tathmini na usanifu daraja hilo ili liweze kutengewa fedha kadri ya upatikanaji wa fedha na kuweza kujengwa ili liweze kurejesha huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kushirikiana na Halmashauri ya Busokelo na Mheshimiwa Mbunge ili kuweza kuona namna gani usanifu unafanyika na fedha zinatafutwa na kujenga daraja hilo kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba kabla barabara hazijajengwa tunatengeneza bajeti, tukishaipitisha ndiyo inaanza kutekelezwa. Wakati mwingine kuna miradi ambayo inatokana na majanga, mfano barabara imekatika ghafla na yenyewe haikuwa imetengewa fedha, lakini kila ukiomba fedha inakuwa ni maneno tu wala hazipatikani.

Sasa nataka kufahamu, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba tunapopata majanga kama madaraja yanapokatika, wa kutoa fedha za dharura ili kuyajenga kuliko hivi ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ujenzi wa barabara zetu unatekelezwa kwa mujibu wa bajeti za Serikali. Pia unatekelezwa kwa mujibu wa mapato yanayopatikana kutokana na makusanyo mbalimbali ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utaratibu wa kutenga bajeti na kuandaa fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizo lakini pia utayari wa Serikali kuhudumia majanga pale yanapojitokeza na kukata mawasiliano ni jambo ambalo linapewa kipaumbele sana na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninachoomba ni kupata taarifa rasmi kutoka katika jimbo lake kwa hiyo barabara na daraja husika ili wataalam wa TARURA katika eneo husika na ngazi ya Wizara tuweze kuona namna ya kufanya thamini na usanifu na kutafuta fedha kwa ajili ya kwenda kufanya ujenzi na marekebisho ya daraja husika.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Jimbo la Newala Vijijini linakabiliwa na uhaba mkubwa wa upatikanaji wa dawa kwa wananchi wake. Je, Serikali inasema nini kuhusiana na suala hili? Uhaba ule unachangia kwa kiasi kikubwa sana wananchi kushindwa kujiunga na mpango wa CHF iliyoboreshwa kwa sababu wamekatishwa tamaa na mpango wa awali, wakienda vituoni hawapati dawa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Jimbo la Newala Vijijini linakabilishwa na uhaba mkubwa pia wa watumishi, hali ambayo inazorotesha utoaji wa huduma za afya kwa wananchi. Ni lini Serikali itapeleka watumishi wa afya katika Jimbo la Newala Vijijini ili wananchi wale wapate huduma inayostahili kama wananchi wengine? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeweka kipaumbele kuhakikisha vituo vyetu vya huduma kote nchini vinakuwa na dawa za kutosha. Ndiyo maana katika kipindi cha miaka mitano, bajeti ya dawa ya Serikali imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015 hadi shilingi bilioni 271 mwaka 2020. Hii ni jitihada kubwa sana ya Serikali kuhakikisha wananchi wanapata dawa za kutosha vituoni.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusisitiza, kwanza kuhakikisha Halmashauri zinasimamia ipasavyo mapato ya uchangiaji wa huduma za afya katika vituo vyetu. Nasi Waheshimiwa Wabunge ni sehemu ya Madiwani katika Halmashauri zetu, kumekuwa na changamoto ya usimamizi wa makusanyo ya fedha za uchangiaji ili ziweze kuongeza mapato ya vituo na kuboresha dawa katika vituo vyetu. Serikali itaendelea kusimamia kwa karibu na kuboresha upatikanaji wa dawa nchini kote lakini katika Halmashauri ya Newala Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na uhaba wa watumishi, Serikali imeendelea kutoa kipaumbele cha hali ya juu sana katika kuboresha upatikanaji wa watumishi katika vituo vyetu. Mipango iliyopo ni pamoja na kuendelea kuajiri na ushahidi unaonekana. Katika kipindi cha miaka mitano, zaidi ya watumishi 14,000 na mwaka jana madaktari 1,000 wameajiriwa katika vituo vyetu mbalimbali. Zoezi hili la kuajiri watumishi wa afya ni endelevu na Serikali itaendelea kuajiri ili kuboresha huduma za afya katika nchi yetu.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, imekuwa ni ahadi ya muda mrefu ya ujenzi wa sehemu za kujisubiria akina mama hasa wajawazito. Tumesema katika sera kwamba tutakuwa na Vituo vya Afya katika kila Kata na Zahanati katika kila kijiji; lakini katika Jimbo la Kalenga hii imekuwa ni changamoto kubwa sana. Akina mama wakijifungulia njiani wanatozwa Sh.50,000/= mpaka Sh.70,000/=. Ni lini Serikali itajenga majengo ya kujisubiria katika Jimbo hili la Kalenga? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nini kauli ya Serikali kuhusu hizo tozo ambazo zinatozwa kwa akina mama ambao pia ni walipa kodi katika nchi hii na Serikali ndiyo yenye changamoto ya kutojenga hivyo Vituo vya Afya? (Maikofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Tendega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunahitaji kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga kwa kuboresha miundombinu ya huduma za afya. Ni kweli kwamba miradi ya ujenzi wa majengo ya kujisubiria kwa maana ya maternity waiting homes, imekuwa ni kipaumbele cha Serikali. Hata hivyo, majengo hayo yanajengwa ili kupunguza umbali wa wajawazito kufika kwenye Vituo vya Huduma za Afya. Kwa hiyo, ili ujenge majengo haya ni lazima uwe na Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Spika, sasa kupanga ni kuchagua. Ndiyo maana Serikali imepanga kwanza kujenga kwa wingi Vituo vya Afya ili viwe karibu zaidi na makazi ya wananchi na tuweze sasa, yale maeneo ambayo yana umbali mkubwa, kuweka mpango wa pili wa kuanza kujenga majengo ya kujisubiria wajawazito. Haitakuwa na tija sana ukiwekeza kujenga majengo ya kujisubiria wananchi sehemu ambayo ina umbali mkubwa sana kutoka kwenye vituo vya huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kipaumbele namba moja ni lazima uwe na kituo, ndiyo maana yale majengo yanajengwa karibu na kituo. Ndiyo maana katika miaka hii mitano tumejenga vituo vingi na tunaendelea na ujenzi wa vituo hivyo ili kusogeza huduma kwa wananchi, hatimaye tutakuja kujenga sasa majengo ya kusubiria wajawazito. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kipaumbele hicho bado kipo, lakini tunaboresha kwanza vituo na baadaye tutakenda kwenye awamu wa ujenzi wa majengo ya kujisubiria.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kauli ya Serikali kuhusu tozo, Serikali haijatoa maelekezo yoyote kwa watendaji na watoa huduma kutoza faini kwa wajawazito wanaojifungulia majumbani.

Mheshimiwa Spika, ni wajibu wa watendaji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, ni wajibu wa watumishi katika vituo vya huduma kutoa elimu na kuhamasisha wajawazito kuona umuhimu wa kujifungulia katika vituo vya huduma badala ya kuwalipisha faini wakijifungulia nje ya vituo vya huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali itaendelea kusimamia jambo hilo. Naomba nitoe wito kwa watendaji wote kuzingatia jukumu lao la kutoa elimu na kuhamasisha wananchi kujifungua katika vituo vya huduma.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hospitali nyingi zinatoza wanawake wajawazito wanapokwenda kujifungua. Hospitali ya Kitete ni moja kati ya Hospitali ambazo zinatoka akina mama; anapojifungua mtoto wa kiumbe analipa Sh.50,000 na anapojifungua mtoto wa kike, analipa Sh.40,000. Je, Serikali imeweka tozo hii kwa ajili ya nini? (Kicheko/Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utoaji wa huduma za afya nchini unatolewa kwa mujibu wa sheria, sera na miongozo ikiwemo utoaji wa huduma za afya kwa wajawazito wakati wa kujifungua. Serikali imeelekeza bayana kwamba huduma za wajawazito na watoto wa chini ya umri wa miaka mitano zinatolewa bila malipo yoyote na Serikali inaendelea kusimamia utekelezaji wa sera na miongozo hiyo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba baadhi ya maeneo, kwa baadhi ya watumishi wasio waaminifu, kwa namna moja ama nyingine wamekuwa wanatekeleza kinyume na sera na mwongozo huo. Kazi ya Serikali ni pamoja na kupokea maoni ya Waheshimiwa Wabunge na kuyafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niyachukue mawazo ya Mheshimiwa Mbunge na niwahikikishie kwamba tutaenda kuyafanyia kazi ili kuondokana na changamoto hiyo. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza kabisa naipongeza Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kwa kutupatia pesa shilingi bilioni 5.4 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Wilaya ya Bariadi, Bariadi DC, Itilima na Busega. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali la nyongeza; kwa kuwa tuna upungufu mkubwa wa watumishi katika hospitali zetu hizo za Wilaya nilizozitaja, je, ni lini Serikali itatuletea watumishi wa kutosha hasa madaktari bingwa wa magonjwa ya wanawake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya ujenzi wa miundombinu ya hospitali, vituo vya afya na zahanati, Serikali imeweka mkakati ambao tayari umeanza kutekelezwa wa kuajiri watumishi wa kada za afya kuanzia madaktari na wauguzi na ajira hizi zinatolewa kwa awamu. Lengo la ajira hizi ni kwenda kuhakikisha majengo yote yaliyojengwa yanatoa huduma bora za afya kama ilivyotarajiwa.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo ni kipaumbele cha Serikali na itaendelea kuajiri wataalam wa afya kadri ya upatikanaji wa fedha ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi katika Halmashauri za Mkoa wa Simiyu na nchini kote.
MHE. EDWARD K. OLELEKAITA: Nakushukuru, kwa kuwa swali lililoulizwa linafanana kabisa na matatizo na changamoto tunayopata kama Wilaya ya Kiteto, hususan Hospitali ya Wilaya, tuna upungufu wa mashine ya x-ray, jenereta ni mbovu, majengo, gari la kubeba wagonjwa, vitanda na mashine ya usingizi. Ni lini sasa Serikali itapeleka vifaa hivi katika Hospitali yetu ya Wilaya ya Kiteto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Olelekaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu ya utoaji wa huduma za afya yakiwemo majengo, vifaatiba, x-ray, ultra sound na vifaa tiba vingine ni vifaa ambavyo vimepewa kipaumbele katika vituo vyetu vya huduma ili kuweza kufikisha huduma bora kwa wananchi na ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeeleza jinsi ambavyo Serikali imetenga fedha kiasi cha takribani bilioni 33.5 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali zetu 67 za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ni kuhakikisha tunaendelea kuboresha upatikanaji wa vifaa tiba katika vituo vyetu vyote ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Kiteto.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tunapozungumzia Hospitali ya Wilaya hatuzungumzii majengo bali tunazungumzia huduma inayotolewa kulingana na level ya Wilaya. Ninapenda kujua Serikali ni lini itatuletea watumishi wa kutosha pamoja na vifaatiba katika Hospitali ya Wilaya ya Nkasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, uboreshaji wa miundombinu na watumishi katika vituo na hospitali zetu za Halmashauri ni kipaumbele cha Serikali na utekelezaji wake unafanyika kwa awamu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na ndiyo maana katika mipango ya Serikali ya kila mwaka Serikali inatenga fedha, kwanza, kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaajiri watumishi ili kuondoa changamoto ya watumishi katika hospitali na vituo vyetu. Lakini pili, tunatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaboresha upatikanaji wa huduma bora za afya katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua sana kwamba majengo ni kitu kingine na huduma bora ni kitu muhimu pia na ndiyo maana tumeendelea kuboresha miundombinu hiyo, lakini upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na watumishi na tutaendelea kuhakikisha kwamba tunatekeleza suala hilo.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, natambua kwamba Serikali inafanya jitihada kubwa sana kupunguza umaskini vijijini; na kwenye vijiji vyetu vingi vyanzo vya mapato ni vidogo na hivyo kusababisha mikopo ya halmashauri kuwa midogo vijijini ukilinganisha na mijini. Je, Serikali haioni kama kuna haja ya kutafuta njia sahihi ya kugawa mikopo hii ili basi kutimiza dhima hii ya Serikali? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; akina mama wa Arusha Mjini wamenituma, sasa hivi kuna sintofahamu ya kugawa mikopo katika Wilaya ya Arusha Mjini. Wanalazimishwa waanzishe viwanda vidogo vidogo ndipo wapate mikopo ya Halmashauri. Akinamama wa Arusha Mjini ni akinamama hodari sana na wanajishughulisha na shughuli nyingi zikiwemo kilimo, ufugaji na hata utalii, wanauza vinyago na shanga na shughuli zingine kadhalika. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu jambo hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba halmashauri zetu zinatofautiana uwezo wa ukusanyaji wa mapato na hasa Halmashauri za mijini ikilinganishwa na Halmashauri za vijijini. Ni lengo la Serikali kuwawezesha wajasiriamali wa vikundi tajwa kwa maana ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni jambo ambalo linahitaji tafakari ya karibu zaidi kuona uwezekano wa kuweka kiwango sawa kwa Halmashauri zote kwa sababu pia halmashauri hizi idadi ya wananchi inatofautiana. Unaweza ukatafakari kwa mfano tukisema tuweke kiasi sawa kwa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kwa mfano kwa idadi ya wananchi waliopo na Halmashauri ya Wilaya ya Ileje kwa mfano kwa idadi ya wananchi waliopo. Ni dhahiri kwamba Manispaa na Majiji na Miji zina idadi kubwa zaidi ya wananchi na hivyo ni rahisi kuwa na vikundi vingi zaidi kuliko vijijini.

Kwa hiyo, mgawanyo unaotolewa kwa asilimia 10 ya mapato ni equitable inategemeana pia na makusanyo, lakini pia hata idadi ya wananchi katika maeneo hayo inatofautiana. Lakini ni jambo muhimu, tunalichukua na tutaendelea kulifanyia kazi kuona namna bora zaidi ya kuboresha ili wananchi hawa waweze kupata faida ambayo imekusudiwa na Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na sintofahamu ya mikopo Arusha Mjini, ninaomba nitoe ufafanuzi kwamba lengo la mikopo ya asilimia 10 ni kuwawezesha makundi hayo katika shughuli zao za ujasiriamali na maelekezo yaliyotolewa ni wao kuunda vikundi hivyo, lakini pia kutafuta shughuli za ujasiriamali ambazo zinawaingizia mapato na kusajiliwa ili waweze kupata mikopo hii.

Kwa hiyo, hakuna utaratibu wa kulazimisha vikundi vya wanawake, vijana au watu wenye ulemavu kufanya shughuli maalum ili waweze kupata mikopo na ninaomba niendelee kusisitiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuzingatia utaratibu na kanuni za utoaji wa mikopo bila kulazimisha wajasiriamali. (Makofi)
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa majibu ya Serikali yameeleza bayana kwamba uwiano wa mapato katika kila Halmashauri ni tofauti na hata wingi wa watu ni tofauti; na kwa kuwa shida hii ya mikopo ya akinamama bado inaonekana ni kubwa; je, ni lini Serikali itakuwa tayari sasa kuongeza asilimia ya mikopo kwa akinamama kutoka asilimia nne kwenda asilimia 10? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna uwiano tofauti wa mapato ya ndani ya Halmashauri, lakini hoja ya kuongeza kiwango cha ukopeshaji kutoka asilimia 10 kwenda juu zaidi ni jambo ambalo linahitaji kufanyiwa tathmini na kuona uwezekano wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majukumu haya ya asilimia 10, ikumbukwe pia mapato ya Halmashauri yanahitajika pia kuboresha miundombinu mbalimbali kama ujenzi wa vituo, ukarabati wa madarasa, ujenzi wa madarasa na huduma mbalimbali za wananchi. Kwa hiyo, ni jambo ambalo linahitaji pia kufanyiwa tathmini kuweza kuona faida zake na kuweza uona namna gani litaboresha huduma kwa ujumla katika halmashauri na katika vikundi hivi husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba niseme tunachukua wazo la Mheshimiwa Mbunge, tutalifanyia tafakuri na kuona njia bora zaidi ya kuboresha mfumo huu wa utoaji wa mikopo ya asilimia 10. (Makofi)
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nia ya mfuko huo ni kujaribu kusaidia vijana na akina mama na watu wenye ulemavu katika kukuza ajira, hawaoni sasa ni muda mwafaka wa kuongeza muda kutoka miaka 18 hadi 45 badala ya 18 mpaka 35 ambayo hiyo inawazuia wananchi walio wengi kupata mikopo hiyo na kufanya biashara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la mikopo hii kwa vijana ni kuhakikisha kwamba pia inawawezesha kiuchumi, na hasa vijana wa umri wa miaka 18 hadi 35 kwa maana ya definition ya kijana. Kwa hiyo, wazo lake la kuongeza wigo kutoka miaka 18 hadi 45 linahitaji pia kulifanyia tathmini na kuona kama miaka 45 iko ndani ya umri wa ujana au kama maana yenyewe ya vijana inahitaji kuboreshwa ili kuongeza wigo huo. Kwa hiyo, ni wazo zuri, lengo ni kuboresha na sisi Serikali tunaomba tulichukue hilo tukalitafakari na kuona uwezekano wa kulitekeleza kwa manufaa ya jamii yetu. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ukweli Halmashauri za Tanzania hazilingani upande wa vyanzo vya mapato, na kwa kuwa Halmashauri kama ya Wilaya ya Same vyanzo vya mapato ni vya chini mno, kwa hiyo, inasababisha wananchi wa Wilaya yetu wa Same kuwa maskini ukilinganisha na kwenye Wilaya nyingine ambazo wana vyanzo vikubwa vya mapato.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutafuta taratibu nzuri ya kufanya zile Halmashauri ambazo vyanzo vya mapato viko chini mno nao wakaongezewa ili wananchi wa Tanzania wawe katika uwiano unaolingana? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tofauti ya kiwango cha mapato katika Halmashauri inatokana na wigo wa ukusanyaji wa mapato katika Halmashauri husika na kimsingi asilimia kumi kama ambavyo jibu la msingi limeeleza, linatokana na mapato ya ndani baada ya kutolewa vyanzo lindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali inaona umuhimu wa kuona namna gani tunaweka mazingira mazuri zaidi kwa Halmashauri zile ambazo zina mapato ya chini zaidi, lakini jambo hili linahitaji kulifanyia tathmini, kulipitia na kuona njia nzuri zaidi ya kuendelea kuboresha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue wazo la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, kuweza kuona ni namna gani tunafanya ili tuweze kuboresha huduma hizi za mikopo ya asilimia 10. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninalo swali la nyongeza.

Kwa kuwa asilimia hizi zipo kisheria na bado kuna ukakasi katika mgawanyo huu; je, yupo tayari sasa kuja kuona uhalisia wa suala lenyewe katika Jimbo la Mbulu Mji na Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kushirikiana naye na Halmashauri ya Mbulu kuweza kuona namna gani tunatatua huo ukakasi ambao Mheshimiwa Mbunge ameuripoti uliotokana na mgawanyo wa mali kati ya Halmashauri ya Mbulu Vijijini na Halmashauri ya Mbulu Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba baada ya Mkutano huu wa Bunge tutapanga tuone utaratibu mzuri wa kuwaza kutatua changamoto hiyo. (Makofi)
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali.

Kwa kuwa bajeti inayoendelea sasa tuko robo ya tatu na Serikali ilitenga shilingi milioni 750, ni lini Serikali itazileta hizi fedha za bajeti ya mwaka huu unaoendelea ili tuweze kuendelea na ujenzi wa jengo hilo la Halmashauri? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa jengo hili ni la muda mrefu na Serikali imewekeza fedha nyingi za kutosha na ili ufanisi wa shughuli za Halmashauri uweze kwenda vizuri, je, mwaka huu wa fedha Serikali itatenga fedha za utoshelevu ili kuhakikisha kwamba jengo hili linakamilika na majengo mengine ambayo yako kwenye nchi hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniventura Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu kwenye swali la msingi kwamba Serikali kwa mwaka huu wa fedha 2020/2021 imekwishatenga shilingi milioni 750 kwa ajili ya kufanya shughuli za umaliziaji wa jengo la utawala katika Halmashauri ya Magu. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Magu kwamba fedha hizo ziko katika hatua za mwisho za kutolewa ili ziweze kufikishwa katika Halmashauri hiyo kwa ajili ya kutekeleza shughuli hizo zilizokadiriwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na jengo hili kuwa la muda mrefu ni kweli na Serikali inatambua kwamba jengo hili lina muda mrefu tangu limeanza kujengwa, na dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwamba linakamilika mapema iwezekanavyo na ndiyo maana katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha Serikali itatenga kiasi cha shilingi bilioni moja na milioni mia moja kwa ajili ya jengo la utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Magu. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itatenga fedha hizo na zitafikishwa ili ziweze kukamilisha jengo hilo kwa ajili ya kuboresha huduma kwa wananchi.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mtama tulipokabidhiwa Halmashauri hii na Mheshimiwa Rais alituahidi kwamba ujenzi wa mjengo yake utaanza mapema na hivi karibuni Waziri Mkuu alifanya ziara Jimboni Mtama na kutuahidi kwamba hizi fedha za ujenzi zitakuja.

Sasa je, Serikali iko tayari kuanza kuleta hizi fedha hata kama ni kwa awamu ili ujenzi huu na ahadi ya Mheshimiwa Rais ianze kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye, Mbunge wa Mtama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imedhamiria kuhakikisha inakamilisha au inaanza ujenzi wa majengo ya utawala katika Halmashauri zile mpya ambazo miongoni mwao ni Halmashauri hii ya Mtama.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka huu wa fedha jumla ya shilingi bilioni 80.42 zimetengwa na zitaanza kutolewa wakati wowote kuanzia sasa na taratibu zinaendelea ili zile Halmashauri ambazo kwanza zilipata fedha za kuanza ujenzi zipate fedha kwa ajili ya kukamilisha majengo hayo lakini zile ambazo zinahitaji kuanza ujenzi ziweze kupata fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa majengo ya utawala.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili katika mwaka wa fedha ujao pia Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha shughuli hizo za ujenzi wa majengo ya utawala zinakamilika. Kwa hivyo, naomba nimhakikishie Mbunge wa Mtama, Mheshimiwa Nape kwamba Serikali inatambua uhitaji wa kuanza ujenzi wa jengo la utawala katika Halmashauri ya Nape hiyo ya Mtama na tutahakikisha fedha zinatengwa kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huo. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Naishukuru Serikali kwa kuwa na mpango wa kujenga Hospitali ya kisasa kwenye Mkoa wetu wa Morogoro. Hata hivyo, bado kuna tatizo la umilikishaji na nimeambiwa kuwa karibu watakamilisha umilikishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, Hospitali hiyo ya Rufaa ya Morogoro ambayo tunaipanua mpaka sasa hivi haina kifaa cha CT-Scan na hili swali nilishauliza humu ndani, nikaahidiwa lakini mpaka sasa hivi hatujapata kifaa hicho. Je, kifaa hicho tutapatiwa lini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, kutokana na Mkoa wa Morogoro kuwa katikati na kupokea majeruhi wengi lakini tuna tatizo la mtambo wa oxygen. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutupatia mtambo wa oxygen ili kupunguza matatizo tuliyonayo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imedhamiria kuhakikisha inaboresha huduma za afya za kibingwa katika Hospitali za Rufaa za Mikoa ikiwepo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro. Katika mipango yake, Serikali imeweka mipango ya kuhakikisha vifaa tiba kama CT-Scan zinapatikana katika hospitali kubwa za mikoa ikiwemo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali iliahidi na ahadi yake bado ipo pale pale. Kazi inayoendelea sasa ni kutafuta fedha ili tuweze kupata mashine hiyo ya CT- Scan na kuifunga katika Hospitali ile ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ili kuweza kuboresha huduma. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo bado linafanyiwa kazi na Serikali na litakamilika ili tuweze kuboresha huduma za afya katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na umuhimu wa kuwa na mtambo wa oxygen katika hospitali ile, ni kweli, Mkoa wa Morogoro upo kwenye highway ambapo mara nyingi kunakuwa na matukio ya ajali. Kwa hiyo, tuna kila sababu ya kuwa na mitambo ya oxygen ili kuwezesha mkoa kuwa na uhakika wa kupata oxygen pale inapohitajika. Jambo hili pia limechukuliwa na Serikali, linafanyiwa kazi, fedha inatafutwa ili mtambo uweze kuwekwa pale na kuboresha huduma kwa wananchi.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa kule kwetu Namtumbo kuna vituo vya afya viwili; Kituo cha Afya cha Mkongo na Kituo cha Afya cha Mputa ambavyo vilijengwa mwanzoni mwa miaka 1980 na hali yake kwa sasa hivi ni mbaya sana.

Kwa kuwa wakati ule vilipojengwa kulikuwa hakuna majengo ya upasuaji, je, Serikali inaweza ikatusaidia kutuletea au kututengea fedha kwa ajili ya kukarabati vituo hivyo vya afya na kujengewa vyumba vya upasuaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya utoaji huduma za afya na kwa muktadha huu inajumuisha ujenzi wa vituo vya afya, upanuzi na pia ukarabati vituo vya afya. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo, Kituo cha Afya cha Mkongo na Mputa ni Vituo vikongwe na vinahitaji kufanyiwa upanuzi na vinahitaji kukarabatiwa na kuongezewa baadhi ya majengo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kwamba Serikali inachukua hoja hii na kwenda kuifanyia kazi ili tuweze kuona kadri ya upatikanaji wa fedha, tunatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa vituo hivyo na pia kuongeza majengo; yakiwepo ya upasuaji na majengo mengine ili viweze kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Pamoja na kazi kubwa na nzuri iliyofanywa na Serikali kwenye ujenzi wa hospitali na vituo vya afya, kama alivyokiri Mheshimiwa Naibu Waziri, ni kweli bado kuna uchakavu mkubwa wa vituo vyetu vya afya.

Napenda kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, ni upi sasa mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tunamaliza kabisa ukarabati wa vituo vyote vichakavu na vikongwe vikiwemo Vituo vya Afya vya Mombo, Bungu na Magoma katika Wilaya ya Korogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imefanya kazi kubwa sana katika ujenzi wa hospitali, vituo vya afya na zahanati na pia imefanya kazi kubwa sana katika kukarabati vituo vya afya ili kuwezesha kutoa huduma bora kwa wananchi. Ni kweli pia kwamba bado kazi ipo na inahitajika kufanyika zaidi na Serikali inatambua kwamba bado kuna vituo vya afya ambavyo ni chakavu na vinahitaji kukarabatiwa vikiwemo vituo vya afya vilivyopo katika Jimbo la Korogwe Vijijini kwa Mheshimiwa Mnzava.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka huu, Serikali imetenga shilingi bilioni 11 na imeshaainisha hospitali 43 za Halmashauri kwa ajili ya ukarabati na kuongeza majengo ambayo yanapungua ili yaweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi. Pia mchakato wa kuandaa na kuainisha vituo vya afya chakavu vikiwemo vya Korogwe Vijijini, unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mnzava kwamba vituo vyake pia vitaingizwa katika orodha hiyo ili kadri ya upatikanaji wa fedha viweze kukarabatiwa na kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha za kutosha kuweza kukarabati na kujenga wodi ya akina mama katika hospitali ya Wilaya ya Mangaka. Hospitali ile imekwisha, je, Serikali inatuhakikishia vipi upatikanaji wa vifaa tiba katika hospitali ile wakati kazi imeshakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetenga bajeti ya kununua vifaa tiba katika hospitali zote mpya za Halmashauri
67. Jumla ya shilingi bilioni 33.5 zimetengwa katika mwaka huu wa fedha na tayari taratibu za mawasiliano kati ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Afya na MSD kuona utaratibu wa kupata vifaa tiba katika hospitali zile mpya unafanyika mapema iwezekanavyo ili vifaa vile viweze kupelekwa katika hospitali zetu mpya za Halmashauri na kuanza kutoa huduma zinazotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mhata na Waheshimiwa Wabunge kwamba hospitali zetu zote na vituo vya afya zilizojengwa, taratibu za kuhakikisha zinaanza kutoa huduma za afya zinaendelea na Serikali inaendelea kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha, kutenga fedha za kununua vifaa hivyo ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Nanyumbu.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, na kutakuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kuuliza, kwa kuwa suala la kupanuliwa kwa hospitali hiyo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais kwa muda mrefu; je, hospitali hiyo iko kwenye idadi ya hospitali 21 zitakazokarabatiwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kwa kuwa, hospitali hiyo inatoa huduma kwa akina mama na watoto vijijini ambao hawana uwezo wa kupata huduma za afya kwenye hospitali binafsi ambazo ni gharama kubwa, je, Serikali sasa haioni ni wakati muafaka wa kuiweka hospitali hiyo kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022 ili na yenyewe iweze kutoa huduma bora kwa wananchi wetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Noah Mollel Mbunge wa Arumeru Magharibi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimhakikishie kwamba ahadi zote za viongozi wetu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Nimhakikishie kwamba hospitali hii ya Orturmet ni miongoni mwa hospitali ambazo zimepewa kipaumbele; na nimhakikishie kwamba katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 tumeanza na hospitali 21 awamu ya kwanza; na tutakuwa na awamu ya pili ya hospitali zile nyingine ambazo zinabaki. Nimhakikishie katika awamu hiyo ya pili hospitali hiyo ya Orturmet Arusha ni miongoni mwa hospitali ambazo zitaingizwa ili ziweze kufanyiwa upanuzi na ukarabati.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hospitali hii inatoa huduma kwa wananchi vijijini na wengi wao ambao hawana uwezo na ndiyo maana Serikali imeendelea kuhakikisha kwamba inaingiza kwenye orodha hospitali ambazo zinapewa kipaumbele kwaajili ya ukarabati ili iendelee kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi katika maeneo hayo. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Noah kwamba jambo hilo linafanyiwa kazi na mara fedha zikipatikana hospitali hii itakarabatiwa ili iweze kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa, Kata ya Iyumbu ipo pembezoni na haina kituo cha afya wala zahanati katika vijiji vyake vyote, je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo cha afya katika Kata ya Iyumbu iliyopo Jimbo la Singida Magharibi ili kuwawezesha wananchi wake kupata huduma bora za afya na kuokoa vifo vya akina mama na Watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aysharose Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunafahamu pamoja na jitihada kubwa na kazi kubwa sana iliyofanywa na Serikali ya kujenga vituo vya afya, ambapo katika miaka mitano iliyopita zaidi ya vituo vya afya 490 vimejengwa bado kuna uhitaji wa vituo vya afya katika kata zetu mbalimbali kote nchini. Kwa hiyo katika eneo hilo Kata hii ya Iyumbu katika Mkoa wa Singida ni miongoni mwa kata ambazo kimsingi zina uhitaji wa kituo cha afya.

Mheshimiwa Naibu Spika na Mpango wa Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo ya Afya Msingi ni kuendelea kujenga vituo vya afya kwa awamu katika kata zetu kadri ya upatikanaji wa fedha. Mimi naomba nimhakikishie Mheshimiwa Aysharose kwamba tunachukua hoja hiyo, na kadri ya upatikanaji wa fedha tutaendelea kutoa kipaumbele katika Kata hii ili tuweze kujenga kituo cha afya na kuweza kuwahudumia wananchi ipasavyo.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa hospitali ya Makandana wilaya ya Rungwe imeshajengewa wodi ya wanawake. Serikali ina mpango gani wa kutuongezea madaktari bingwa wa magonjwa ya wanawake katika hospitali ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeboresha miundombinu katika hospitali ya Wilaya ya Rungwe, hospitali ya Makandana kwa kujenga wodi ya wanawake ili kuendelea kuboresha huduma za afya ya mama na mtoto katika Halmashauri ya Rungwe. Ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba bado Serikali ina mipango ya kuendelea kuboresha miundombinu hiyo ikiwemo kuongeza vifaatiba lakini pia kuongeza madaktari.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimhakikishie kwamba kwa sera na miongozo kwa sasa hospitali zetu za Halmashauri bado hazijawa na mwongozo wa moja kwa moja wa kuwa na waganga mabingwa, kwa maana ya madaktari bingwa katika hospitali hizo, kwa sababu kwa ngazi ile madaktari wa ngazi wanaopatikana bado wana uwezo mzuri wa kutibu na tuna mfumo mzuri wa rufaa pale ambapo kuna kesi ambazo zinashindikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Sophia Mwakagenda kwamba Serikali itaendelea kuboresha ikama ya madaktari katika hospitali ya Makandana ili waendelee kuhudumia vizuri wananchi wetu wakiwepo wanawake katika wodi hizo na kwenda kuboresha huduma za afya kadri ya matarajio ya wananchi.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Jimbo letu la Mkinga lina vituo vya afya viwili tu. Kituo cha kwanza ni Kitomanga na kituo cha pili ni Rutamba. Kituo cha Rutamba kipo katika hali mbaya sana. Hakikidhi haja za kutoa huduma za afya kama kituo.

Je, ni lini Serikali itatutengea pesa kwa ajili ya ukarabati wa kituo hicho? Kama itampendeza Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri naomba nifuatane nae akaone hicho kituo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa mama Salma Kikwete Mbunge wa Mkinga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika Jimbo la Mkinga kuna upungufu mkubwa wa vituo vya afya na vituo vya afya vilivyopo ni chakavu ikiwepo Kituo cha Afya hiki cha Mtamba. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mama Salma Kikwete kwamba Serikali inatambua kwamba kuna uhitaji mkubwa sana wa vituo vya afya katika Jimbo la Mkinga na ninatambua kwamba kuna kila sababu ya kuweka jitihada za maksudi kuhakikisha tunakarabati Kituo cha Afya cha Mtamba ili kiweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nichukue nafasi hii kumhakikishia kwamba tutachukua hoja hii na kuiwekea kipaumbele katika awamu inayokuja ya ukarabati wa vituo vya afya ili kituo hiki pia kiweze kuwekewa fedha kwa ajili ya ukarabati na upanuzi ili kitoe huduma bora za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa mama Salma Kikwete kwamba tutaendelea kushirikiana kwa karibu sana, na Ofisi ya Rais TAMISEMI tuko tayari wakati wowote kushirikiana na kufuatana na Mheshimiwa mama Salma Kikwete. Baada ya kikao hiki tutapanga kuona uwezekano wa kupata fursa hiyo ili twende kushirikiana pale muda ambapo utaturuhusu.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hospitali ya Kyela jengo la mama na mtoto liliungua. Je, ni lini Serikali sasa itamalizia pesa zilizobaki kwa ajili ya jengo la mama na mtoto katika hospitali ya Kyela?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUNGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mlaghila Jumbe Mbunge wa Kyela kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimhakikishie Mheshimiwa Jumbe kwamba hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kyela ni moja ya hospitali ambazo nazifahamu sana kwa sababu nimekuwa mganga mkuu wa Kyela kwa zaidi ya miaka tis ana nimekuwa sehemu ya uendelezaji wa miundombinu katika Halmashauri ya Wilaya ya Kyela. Ninafahamu kwamba ni kweli wodi ilipata ajali ya moto na Serikali imesha peleka fedha na kazi za ukarabati wa wodi ile zinaendela.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimhakikishie kwamba katika Mpango ujao tumetenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakamilisha ukarabati wa wodi ile iliyopata ajali ya moto ili iweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Jumbe kwamba jambo hilo linafanyiwa kazi na mara fedha zitakapopatikana basi ukamilishaji wa wodi ile utafanyika ili tuendelee kutoa huduma kama ambavyo tunatarajia.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri ambayo imeweza kunijibu, lakini kiupekee kabisa nataka nitoe angalizo kwa Serikali kwamba Kituo cha Afya Tunduma asikichukulie kama vituo vingine ambavyo viko nje ya mpaka wa Tunduma kwa maana mahitaji yake yanakuwa ni makubwa zaidi, kwa hiyo anaposema kwamba ataweza kupunguza watumishi Tunduma tena awapeleke kwenye hospitali hiyo inayojengwa naona kama bado changamoto itakuwa kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ninapenda niulize maswali yangu mawili ya nyongeza; ni lini hasa Serikali itaweza kuanzisha huduma katika hii hospitali inayojengwa ambayo ameweza kutuonesha kwamba asilimia 82 ya ujenzi imeshafanikishwa. Kwa hiyo, ninatamani kujua ni lini hasa huduma zitaanza kutolewa pale?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ninapenda kufahamu mahitaji ya kituo cha afya kulinga na na nature ya watu wa pale tunahitaji madaktari, na madaktari aliyosema nina uhakika ni hao madaktari wawili ambao wanasubiria Hospitali ya Wilaya ianze kufaya kazi.

Sasa basi ninatamani kujua ni lini hasa Serikali itpeleka madaktari na wauguzi wakunga, siyo wahudumu wa afya kama walivyoweza kuanisha kwenye majibu yao, mahitaji yetu ni madaktari na wauguzi wakunga, specifically hapo ninapenda kupata majibu. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumhakikishia Mheshimiwa Mwandabila kwamba Serikali inakichukulia kwa umuhimu wa hali ya juu sana Kituo cha Afya cha Tunduma kwa sababu ya idadi ya wananchi wanaohudumiwa katika kituo kile na ndiyo maana katika maelezo yangu ya msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali imepeleka watumishi wengi sana, watumishi 22 wa ziada ukilinganisha na ikama ya mahitaji ya kituo cha afya, na hiyo ni dalili kwamba Serikali inajali na kuthamini sana huduma za Kituo cha Afya cha Tunduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba kwa sababu tunaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Mji wa Tunduma, kwa vyovyote vile, idadi ya wagonjwa watakaotibiwa katika kituo cha afya itapungua na wengine watakwenda kutubiwa katika Hospitali ya Mji wa Tunduma itakapokamilika. Kwa hiyo, ile idadi ya wagonjwa ambayo itaondoka Kituo cha Afya cha Tunduma itakwenda kuhudumiwa katika hospitali ya mji na watumishi hawa waliopo. Lakini pia Serikali itakwenda kuajiri watumishi wengine kama ambavyo mpangio upo katika mwaka wa fedha ujao ili tuweze kuongeza watumishi katika hospitali ile ya mji lakini pia katika Kituo cha Afya cha Tundma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Hospitali hii ya Mji wa Tunduma inayojengwa inatarajia kuanza huduma za awali za OPD ifikapo tarehe 27 Aprili, 2021 ili wananchi wetu waanze kupata huduma za awali za OPD wakati shughuli za umaliziaji na ujenzi wa miundombinu mingine inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kwa kuwa Kituo cha Afya cha Nakatunguru pale Ukerewe kilishakamilika kujengwa na kukamilika kwake kutasaidia sana kupunguza mzigo kwenye Hospitali yetu ya Wilaya; ni lini sasa Serikali itapeleka wataalam na vifaa tiba ili Kituo hiki cha Afya cha Nakatunguru kianze kufanya kazi na kusaidia kutoa huduma kwa wananchi wa Ukerewe?

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Jimbo la Ukerewe, Wilaya ya Ukerewe, tayari kituo cha afya kimeshajengwa na kimekwishakamilika na hatua iliyobaki sasa ni kupeleka watumishi na vifaa tiba ili huduma za afya zianze kutolewa katika kituo kile.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Ukerewe kwamba Serikali inatambua na tumeshaweka mipango kwanza kuhakikisha katika Halmashauri ya Ukerewe tunapata watumishi wachache kwa maana ya internal redistribution ya watumishi waliopo na vifaa tiba kwa uchache vilivyopo kwa ajili ya kuanza huduma.

Lakini pili, mpango uliopo katika mwaka wa fedha ujao ni kutenga fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba, lakini pia kadri tutakavyoajiri watumishi, tutawapangia katika Halmshauri ya Ukerewe na katika kituo kile cha afya ili kiweze kutoa huduma bora kwa wananchi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tumelichukua, tunalifahamu na tunalifanyia kazi.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona.

Kwa kuwa katika Jimbo la Vwawa kuna Kituo cha Afya ambacho kimejengwa kwenye Tarafa ya Iyula ambacho kimekamilika karibu miaka miwili iliyopita, lakini mpaka sasa hivi hakina watumishi wa kutosha na hakina vifaa.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba watumishi wa kutosha wanapelekwa na vifaa vya kuweza kuwasaidia kutoa huduma mbalimbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mbunge wa Jimbo la Vwawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba sote tunafahamu kazi kubwa sana iliyofanywa na Serikali yetu katika kuboresha miundombinu ya huduma za afya kwa kujenga vituo vya afya takribani 487 ndani ya miaka mitano iliyopita, lakini harakati hizo za ujenzi zinaendelea katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika maeneo mbalimbali bado tuna changamoto ya idadi ya watumishi wanaohitajika kuanza kutoa huduma, lakini pia tuna changamoto ya vifaa tiba, na ndiyo maana katika mpango wetu wa vituo vya afya katika mwaka wa fedha ujao tunatarajia kuomba takribani shilingi bilioni 22.5 kwa ajili kwanza ya kuhakikisha vituo vyote na hospitali za halmashauri zilizojengwa zinapata vifaa tiba kwa kushirikiana na mapato ya ndani ya halmashauri. Lakini pili, mpango upo wa kwenda kuwaajiri watumishi kwa ajili ya kuwapeleka katika vituo hivyo.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Hasunga na Waheshimiwa Wabunge wote wenye hoja kama hiyo, kwamba Serikali ina takwimu za kutosha za mahitaji ya vifaa tiba katika vituo vyetu vya afya, za mahitaji ya watumishi katika vituo hivyo vya afya na itakwenda kuajiri watumishi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha lakini pia tutakwenda kupeleka vifaa tiba. Kwa hiyo, Mheshimiwa Hasunga nikuhakikishe kwamba kituo hicho cha afya kipo kwenye mpango na tutahakikisha kinaanza kutoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nakushukuru. Napenda kuiuliza Serikali kuhusiana na Kituo cha Afya pale Kigogo ambacho kinahudumia Wilaya tatu za Ubungo, Ilala na Kinondoni yenyewe, lakini tuna shida kubwa ya jokofu la kuhifadhia maiti. Tayari Serikali imeshatupatia jokofu lile, lakini limekaa bila ya kuwekwa katika sehemu husika.

Ni lini Serikali itatujengea eneo ambalo tutahifadhia jogofu lile kwa madhumuni ya kuweza kuwahifadhi wenzetu ambao wanatangulia mbele za haki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Kigogo ni kituo muhimu sana na niseme kwa bahati nzuri, mwanzo wa ujenzi mpaka kinakamilika nilikuwa Mganga Mkuu wa Manispaa ya Kinondoni. Kwa hiyo, nakifahamu vizuri sana kituo kile kwamba ni muhimu na kinahudumia wananchi wengi sana katika Manispaa ya Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie katika Halmashauri ambazo zina mapato mazuri na juzi tulipokuwa na Kamati ya LAAC katika Manispaa ya Kinondoni, sehemu muhimu ambayo tuliona ni mfano wa kuigwa katika nchi yetu ni uwekezaji mkubwa wa fedha za mapato ya ndani katika miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kwa uwezo wa makusanyo ya ndani ya Manispaa ya Kinondoni, kazi ya ujenzi wa chumba za kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya cha Kigogo ni jambo linalowezekana. Naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni waweke mpango wa haraka ili waweze kujenga chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya cha Kigogo. (Makofi)
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa tatizo lililopo katika Hospitali ya Mji wa Tunduma linafanana na Hospitali ya Uhuru iliyoko katika Wilaya ya Chamwino ya ukosefu wa wafanyakazi pamoja na ambulance na hospitali hii iko kwenye eneo ambalo ni la barabarani na linahitaji sana huduma za dharura kwa ajili ya wagonjwa.

Je, Serikali inatoa maelezo gani kuhusiana na upungufu huu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Uhuru inayojengwa katika eneo la Chamwino ni hospitali muhimu sana katika kuboresha huduma za afya katika eneo la Chamwino na Jiji la Dodoma kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Serikali inatambua kwamba tunahitaji kupata kwanza watumishi wa kutosha katika hospitali ile kwa sababu ni mpya, ndiyo inakamilika na vilevile inatambua kwamba tunahitaji kupata vifaa tiba na gari la wagonjwa. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tayari limewekwa kwenye mipango ya utekelezaji ya mwaka wa fedha ujao wa 2021/ 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nimhakikishie kwamba tutakwenda kuhakikisha watumishi watakaoajiriwa watapelekwa katika Hospitali ile ya Uhuru. Tutakwenda kuhakikisha kwamba tunafanya utaratibu wa kupata gari la wagonjwa na vifaa tiba ili hospitali ile ianze kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Wizara, kwanza nawashukuru kwa namna ambavyo wameweza kulifanyia kazi suala hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la nyongeza ni kwamba je, Wizara inajipanga vipi sasa kuandaa wataalam ili tarehe 1 Agosti tutakapokuwa tumekamilisha mradi huu uweze kuanza kazi mara moja, kwa kuwa mradi wenyewe ni wa muda mrefu; na kwa kuwa tumewekeza fedha nyingi pia, isije kukosa wataalam tukaacha tena, ikakaa muda mrefu sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ina-coordinate vipi na Wizara nyingine, kwa sababu hali ya kwenda kule kwenye machinjio yetu, pamoja na miundombinu tuliyoiweka, bado kuna changamoto kubwa sana ya barabara. Tunaomba hilo pia Wizara watuhakikishie wata-coordinate vipi kwa kuwa ni mradi wa kimkakati? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tunafahamu machinjio hii imekaa muda mrefu na ndiyo maana nimeeleza kwamba fedha ambazo zimetengwa zitakwenda kukamilisha ujenzi ifikapo mwezi Agosti, 2021. Hata hivyo, kipaumbele ambacho kimewekwa, moja ni kuhakikisha kwamba vifaa vinavyohitajika kuiwezesha machinjio ile kufanya kazi vizuri pamoja na watendaji kwa maana ya watumishi, wataalam wanaohitajika ni kipaumbele cha Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, utekelezaji wa mradi huu unakwenda sambamba na ukamilishaji wa majengo na mipango ya kuhakikisha kwamba tunapata vifaa kwa ajili ya kuhakikisha machinjio inafanya kazi vizuri na kuhakikisha kwamba watumishi wanapatikana ili huduma ziweze kuendelea. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mambo haya yote yako kwenye mipango yetu na tutahakikisha inapokamilika, inaanza kutoa huduma kama ilivyokusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na barabara, ni kweli ni lazima eneo lile lifikiwe vizuri na barabara kwa sababu tunafahamu machinjio ile ni ya kisasa na lengo letu ni kuboresha huduma katika jamii na kuwezesha Manispaa kupata mapato mazuri. Tutakwenda kuhakikisha tunashirikiana kwa karibu sana na TARURA ili kutenga bajeti ya kuhakikisha kwamba barabara ile inafikika. Barabara hii kama inahudumiwa na TANROADS pia tutawasiliana kwa karibu ili iweze kujengwa, ifike pale ili kuboresha huduma hizo.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Serikali inasisitiza Halmashauri zetu ziweze kujitegemea na kukusanya mapato kwa wingi; Halmashauri ya Jiji la Mwanza ambayo kwa sasa haina machinjio ya uhakika, imetumia fedha za ndani kukarabati pamoja na wadau machinjio ambayo kwa sasa ina uwezo wa kuchinja ng’ombe 200 peke yake na mahitaji ni takribani ng’ombe 800 kwa siku.

Je, Serikali iko tayari sasa kuipa Halmashauri ya Jiji la Mwanza fedha kwa ajili ya kununua mashine zitakazowekwa kwenye mashine mpya ili iweze kufanya kazi, kutoa ajira na kuzalisha mapato kwa wingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imewezesha ujenzi wa machinjio ya kisasa katika Jimbo la Nyamagana kwa lengo la kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma katika jamii na kuiwezesha Halmashauri kupata mapato ya kutosha ili iweze kugharamia shughuli za maendeleo katika Jimbo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba pamoja na kukamilika kwa machinjio ile, bado haijaweza kutumika ipasavyo kuchinja ng’ombe kwa uwezo wake; na kwa sasa inachinja ng’ombe 200 kati ya mahitaji ya ng’ombe 800 kwa siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili tumelichukua. Naomba tukalifanyie kazi ili tuweze kuweka mpango wa kuiwezesha machinjio ile kupata vifaa vya kutosha ili iweze sasa kutoa huduma kwa uwezo unaostahili.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tutalifanyia kazi.
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, swali langu la msingi lilikuwa ni kwamba mfumo huu umeshafika kama alivyosema Mheshimiwa Naibu Waziri, kwenye zahanati 400, lakini tunajua nchi hii ina vijiji takribani 12,000, kwa maana hiyo na zahanati hivyo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa swali langu la msingi ni kwamba zahanati nyingi sasa hawawezi kukusanya kwa kutumia ule mfumo na kinachotokea ni kwamba kunakuwa na upotevu wa mapato. Sasa swali langu la msingi ni je, Serikali haioni kwamba tutumie mfumo wa kawaida wa makusanyo ya kawaida (POS) ili tutoke kwenye upotevu ambao unaendelea sasa hivi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili ni kwamba kumekuwa na tatizo la upatikanaji wa dawa, hasa kwa watu wanaotumia CHF, kichecheo kikubwa imekuwa fedha za papo kwa papo, na hiyo inatokana na hii ya kwamba kuna upotevu wa fedha ambazo sasa mtu anakuwa analipa lakini fedha hazionekani.

Kwa hiyo, swali langu liko hapo, kwamba ni namna gani Serikali sasa inakuja kwamba ikiwezekana sisi tutumie POS kwa ajili ya kukusanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine…

NAIBU SPIKA: Umeshauliza maswali mawili Mheshimiwa.

MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Naibu Spika, connection kidogo, mfumo huu unatumia milioni 14 ku- install…

NAIBU SPIKA: Umeshauliza maswali mawili ya nyongeza, na ndiyo yanayoruhusiwa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imeendelea kuweka mikakati ya kuboresha ukusanyaji wa mapato, matumizi ya dawa, vifaa tiba na vitendanishi lakini pia takwimu za huduma za afya katika vituo vyetu kwa kufunga mifumo ya GoTHOMIS. Na ni kweli kwamba bado kuna zahanati na vituo vya afya ambavyo bado havijafungwa mfumo huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge Nollo kwamba kazi hii ya kufunga mifumo katika zahanati zetu ni endelevu. Kama ambavyo tunafahamu, hatujamaliza kujenga zahanati kwenye vijiji vyetu, na wala hatujamaliza kujenga vituo vya afya katika kata zetu lakini pia Hospitali za Halmashauri katika Halmashauri zetu. Kwa hiyo automatically tutaendelea kutekeleza ufungaji wa mfumo huu katika vituo vipya ambavyo vinaendelea kujengwa lakini pia katika vile vituo ambavyo bado havijajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kutumia mfumo wa POS halitatuwezesha kuboresha huduma za afya, kwa sababu lengo la mfumo wa GOT-HOMIS ni kuwa na taarifa za uhakika za magonjwa, matumizi ya dawa, aina ya matibabu yanayotolewa katika vituo. Kwa utaratibu huo hatuwezi kupata taarifa hizo kwa kutumia mashine za POS. Kwa hiyo naomba nimuhakikishie kwamba kama nilivyotangulia kusema tumeshafunga katika vituo 921 nchini kote, na kila mwaka wa fedha tunaendelea kufunga mifumo hii na tutaendelea kufunga ili viendelee kutoa huduma bora zaidi za afya katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na swali pili, changamoto ya upatikanaji wa dawa kwa baadhi ya vituo. Ni kweli Serikali imeendelea sana kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaa tiba katika vituo vyetu vya huduma. Ukilinganisha hali ya upatikanaji wa dawa mwaka 2015 na 2020/2021 tumepanda kutoka wastani wa asilimia 75 kwa dawa muhimu mpaka wastani wa asilimia 80 hadi asilimia 85 kwa dawa muhimu. Lengo la Serikali ni kufika angalau asilimia 95 kuelekea asilimia 100.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niwaombe Waheshimiwa Wabunge; kwamba sisi ni sehemu ya Madiwani katika Halmashauri zetu, sisi ni wawakilishi wa wananchi katika Halmashauri zetu. Tuendelee kushirikiana na Serikali kusimamia ukusanyaji wa mapato ya uchangiaji wa huduma za afya katika vituo vyetu na kuhakikisha dawa zile kama ambavyo Serikali tunasimamia kwa karibu zinatumika na kuwafikia wananchi wote wakiwepo wanachama wa CHF. Kwa hiyo naomba nimuhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili litaendelea kuboreshwa.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Changamoto ya upatikanaji wa dawa haiko kwenye zahanati na vituo vya afya peke yake bali hata katika Hospitali za Rufaa. Hospitali ya Rufaa ya Kitete Mkoa wa Tabora ni miongoni mwa Hospitali ambazo zinachangamoto kubwa ya upatikanaji wa dawa; na hii inatoka na…

NAIBU SPIKA: Swali, swali!

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA:…je? Serikali ina mpango gani wa kuongeza kiwango cha dawa katika Hospitali ya Rufaa ili iweze kuwapatia wananchi wa Tabora huduma iliyobora ya dawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi tunafahamu kwamba pamoja na uboreshaji wa upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu katika Hospitali za Halmashauri na Hospitali za Rufaa za Mikoa ikiwepo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Tabora kwa maana ya Kitete bado tunachangamoto ya upungufu wa dawa baadhi ya vituo. Ndio maana Serikali imeendelea kwanza kuongeza bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba kila mwaka. Kwa mfano kwa miaka mitano iliyopita tulikuwa na bilioni 30 sasa tuna bilioni takribani 270. Pili, tumeendelea kuboresha sana ukusanyaji wa mapato ya fedha za uchangiaji wa huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba kwanza tunapunguza utegemezi wa vituo vyetu kwa bajeti ya Serikali Kuu kwa kuviwezesha kukusanya vizuri mapato ya uchangiaji lakini pia kununua dawa na vitendanishi vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Hawa kwamba jambo hili Serikali tunalichukua, na tumeweka mpango mkakati wa kwenda kuboresha upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu, zikiwezo Hospitali za Rufaa, ikiwepo Hospitali ya Kitete. Nimhakikishie kwamba tutahakikisha kadri ya bajeti na taratibu ambazo zimepangwa tunaboresha sana upatikanaji wa dawa kwa wananchi wa Tabora na katika Hospitali ya Kitete na nchini kote kwa ujumla.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi ya ukarabati katika hospitali mbalimbali kongwe hapa nchini lakini bado kumekuwa na upungufu mkubwa wa watumishi wa afya.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba mapungufu hayo yanakidhi haja iliyopo kwa maana ya idadi ya watumishi wanaotakiwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ujenzi wa hospitali au ukarabati wa zahanati, vituo vya afya na hizo hospitali ni pamoja na kuhakikisha mambo muhimu ya madawa, vitendanishi vinapatikana katika hospitali zetu. Je, Serikali inahakikisha vipi kwamba upatikanaji wa madawa yote muhimu yanapatikana katika hospitali zetu na katika vituo vya afya na zahanati zetu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa kuwajali na kuthamini sana afya za wananchi imeendelea kujenga vituo vya afya kote nchini na kwa kweli kuna upungufu wa watumishi kwa takribani asilimia 45. Serikali imeweka mipango thabiti ya kuhakikisha tunaendelea kuajiri watumishi katika vituo vya afya, zahanati na hospitali za Halmashauri na ndiyo maana mwezi wa Tano hadi wa Sita tulikuwa na ajira za watumishi wa afya 6,324 na watumishi hao wamekwisha ajiriwa tayari wamepelekwa kwenye vituo vya huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili la kuendelea kuajiri watumishi ni endelevu, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua na itaendelea kuhakikisha kwamba inaajiri watumishi kwa awamu ili kupunguza uhaba wa watumishi katika vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, pili; ni kweli kwa sababu ya ongezeko la vituo vya huduma za afya kumekuwa na upungufu wa baadhi ya dawa muhimu katika vituo vyetu na Serikali imeendelea kupeleka fedha Bohari Kuu ya Dawa mpaka Juni tarehe 30 mwaka huu, jumla ya bilioni 120 zilikuwa zimepelekwa Bohari Kuu ya Dawa kwa ajili ya kununua dawa kupeleka katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha 2021/ 2022 fedha zimetengwa zaidi ya bilioni 280 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba dawa zinapelekwa katika vituo vyetu. Kwa hivyo, nimhakikishie kwamba suala hilo litaendelea kutekelezwa kwa ufanisi unaotakiwa ili dawa zipatikane katika vituo vyetu. Ahsante sana.
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Spika, ninashukuru Serikali kwa majibu mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Serikali imesema kwamba Halmashauri ambazo zitakidhi vigezo zitaanza kunufaika na hiyo hati fungani, sasa ni vigezo vipi ambavyo Serikali imeviweka kwa Halmashauri kuonekana zinakidhi.

Mheshimiwa Spika, pia kwa kuwa zoezi hili linaanza mwaka huu wa fedha, ni Halmashauri ngapi ambazo tayari zimekidhi vigezo.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika swali la msingi, vigezo ni Halmashauri yoyote ambayo ina miradi ya kiuchumi, kimkakati ambayo imefanyiwa upembuzi yakinifu na kuonesha kwamba ina uwezo wa kurejesha fedha na faida. Kwa hiyo, Halmashauri yoyote ambayo itaibua mradi wowote wa maendeleo ambao tayari umefanyiwa upembuzi huo wana uwezo wa kutumia hati fungani ili kushirikisha umma na wadau mbalimbali kupata mtaji na kuwekeza na hatimaye kuhakikisha kwamba wanapata miradi ya maendeleo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, vigezo ndiyo hivyo, ni ile Halmashauri yenye uwezo kwamba miradi yake ina tija na inaweza ikazalisha faida basi watahusika na utaratibu huu wa hati fungani. Ahsante sana.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba kumshukuru pia Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo amekiri Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba mahitaji halisi ya watumishi ni 469 na tulionao ni 162 na mwaka huu wakati Serikali imeajiri ilipeleka watumishi 20 wakati huo huo tunazo tayari zahanati 24 zimekamilika ambazo zimekuwa hazifanyi kazi. Sasa swali langu la msingi lilikuwa ni lini Serikali itahakikisha inapeleka watumishi wa kutosha ili zahanati hizo ambazo tayari zimekwishajengwa ziweze kufanya kazi?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala ya TAMISEMI katika ziara tumethibitisha kwamba hospitali na zahanati ambazo zimefungwa mifumo ya ukusanyaji mapato zinapata pesa nyingi na zinafanya vizuri Zaidi. Kwa nini Serikali haioni jambo hili linaweza kuwa la kipaumbele ili maeneo ambayo yana network jambo hili likafanyika kwa haraka kuliko kuzungumzia zahanati zaidi ya 20 kutenga milioni 20?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Constantine John Kanyasu Mbunge wa Geita Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna upungufu mkubwa wa watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri ya Mji wa Geita na kama ambavyo nimetangulia kujibu kwenye swali la msingi kwamba Serikali inatambua upungufu huu na ndio maana kwenye ajira zilizopita moja ya halmashauri ambazo zilipata kipaumbele cha kuwa na watumishi wa kutosha ni Mji wa Geita. Lakini kwenye ajira zinazofata naomba nimhakiksihie Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kutoa kipaumbele cha kutosha kwa Mji wa Geita ili tuweze kupunguza pengo hili kubwa la watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri ya Mji wa Geita.

Mheshimiwa Spika, pili ni kweli kwamba mifumo ya ukusanyaji wa mapato kwa njia ya kieletroniki ambao ni mfumo uliobuniwa na Serikali yetu wa GOT- HOMIS umeboresha sana mapato ya uchangiaji wa huduma za afya na mpango wa Serikali pamoja na kuelekeza halmashauri kuhakikisha zinatenga fedha za mapato ya ndani kufunga mifumo hii kwenye zahanati, vituo vya afya na ustawi za halmashauri tumeongea na wadau ili kuweka mkakati ambao utakuwa na muda maalum wa kuhakikisha tunashirikiana nao kufunga mifumo hii maeneo yote ambayo inaweza ikatumika na kuboresha mapato. Kwa hivyo suala hili tumelichukua kwa utaratibu huo pia wa kuweka mkakati maalum kabisa na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaenda kulitekeleza, nakushukuru sana.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, upungufu wa vifaa tiba ulioko Geita upo vilevile kwenye hospitali nyingi kama sio zote za wilaya, za mikoa, rufaa katika kukabiliana na janga la Covid - 19 hususan mitungi ya oxygen wananchi wengi wanakufa kwa kukosa mitungi ya oxygen. Sasa nilitaka Serikali iniambie wana mkakati gani wa dharura wa kuhakikisha hospitali hizi zinapata mitungi ya oxygen ili wananchi wenye uhitaji wa oxygen wasife kwa kukosa oxygen?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima James Mdee Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na upungufu wa baadhi ya vifaa tiba katika vituo vyetu na hospitali zetu za kutolea huduma za afya na Serikali katika mida tofauti na katika bajeti tofauti imeendelea kuweka mikakati ya kutosha kwanza kwa kuongeza sana bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba. Kwa mfano katika miaka mitano iliyopita mpaka sasa tumeongeza bajeti kwa zaidi ya mara tisa kutoka bilioni 30 mpaka bilioni 270.

Mheshimiwa Spika, lakini tunatambua kwamba kweli bado kuna changamoto ya vifaa tiba na hususan mitungi ya oxygen kama ulivyotamka na tumeweka mpango mkakati sasa wa kuhakikisha kwamba hospitali zetu za halmashauri zinakuwa na mitambo ya kusindika gesi ya oxygen pia kuhakikisha hospitali za rufaa za mikoa zote nchini zinasimika mitambo ya kuzalisha gesi ya oxygen ili tuweze kuondokana na changamoto ya upungufu wa mitungi hii pia kuhakikisha tunaboresha huduma za afya kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo mpango huu utakwenda kutekelezwa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafanyia kazi hayo ili kuhakikisha tunaboresha huduma za afya, ahsante sana.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa ajira ya mwisho ya watumishi wa vituo vya afya na zahanati iliyotoka iliwachukua baadhi ya watabibu waliokuwa wanafanya kazi kwa mkataba na wengi walipoomba zile ajira walikuwa na nafasi ya kuomba kwamba wabaki wapi. Katika Wilaya yangu ya Longido kuna mmoja aliyekuwa anahudumia zahanati ya Kijiji cha Nondoto ambayo ndio inahudumia kata nzima hakuna nyingine alipoomba kubaki pale alipangiwa kwenda Mtwara. Je, Serikali ina mpango gani wa kuipatia zahanati hiyo mganga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Steven Kiruswa Mbunge wa Longido kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika ajira watumishi ambao wanaomba kuajiriwa na Serikali wanakuwa na option ya kuchagua vituo ambavyo wanakwenda kufanya kazi. Na katika mfumo wa ajira za hivi karibuni ambazo zimefanyika mwezi Mei mpaka Juni watumishi wote wamepangiwa kwenye vituo ambavyo waliomba kupitia mfumo wa kieletroniki wa ajira kwenda kufanya kazi katika vituo hivyo. Na watumishi wote wamepelekwa kwenye vituo ambavyo waliomba kwenda kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge inawezekana tulimwitaji sana mganga huyu katika kituo hicho lakini uchaguzi wake aliomba kituo kingine na ndio maana amepelekwa. Lakini jambo la msingi ni kupata mganga katika zahanati ile na mimi nimelichukua hili tutalifanyia kazi ili kuhakikisha tunapata mganga kwa ajili ya kuendelea kutoa huduma katika zahanati ambayo Mheshimiwa Mbunge ametaja, nakushukuru.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, asante sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yako mazuri nichukue nafasi hii kwanza kabisa kuishukuru Serikali kwa kutupatia kituo hicho katika Kata ya Bunyambo ambayo ilikuwa hatuna kituo cha afya katika Tarafa hii ya Kibondo Mjini tangu tupate uhuru. Lakini hata hivyo Kata hii ya Murungu iko takribani kilometa 31 kutoka Kibondo Mjini ambapo kuna hospitali ya wilaya na ukizingatia kwamba sasa bado tuna kata 8 katika tarafa hii ambazo hazina kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, swali langu la msingi ni lini Serikali itatujengea kituo cha afya katika Kata hii ya Murungu kwa kuzingatia umbali huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ninatambua na Serikali inatambua kwamba tunahitaji kupata kituo cha afya katika Kata ya Murungu na ni ahadi za viongozi wetu wa kitaifa.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Serikali inaendelea kutafuta fedha na mara fedha zikipatikana tutapeleka fedha pale kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya, asante sana. (Makofi)
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nimsahihishe kidogo Naibu Waziri majengo yale yalianza kujengwa mwaka 2012, mwaka 2015 majengo yalikuwa yameshasimama.

Mheshimiwa Spika, Serikali haioni umuhimu wa kutuongezea fedha badala ya bilioni moja ili tuweze kukamilisha majengo yale tuondokane na adha ya kufanyia vikao madiwani na watumishi kwenye maeneo vyumba vidogo sana ambavyo hata hewa nzuri havina. Majengo yale yameshakuwa ni ya muda mrefu mpaka yanatoa ule ukungu wa kijani Serikali haioni umuhimu wa kutuongezea fedha ili tuweze kumaliza kabisa majengo yale ili tuachane nao waendelee kwenye maeneo mengine? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mhesimiwa Spika, nchi yetu ni kubwa na kwenye jibu langu la msingi nimeongea namna ambavyo Serikali imeelekeza nguvu kubwa kwenye ujenzi wa majengo ya utawala kwenye halmashauri takribani 100 hivi sasa. Kwa hivyo, safari ni hatua tumeanza na bilioni na tutaendelea kadri ya fedha zainapopatikana tutakwenda kwa awamu kupeleka fedha hizo ili kukamilisha majengo hayo. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba ni kipaumbele cha Serikali na tutahakikisha tunakamilisha jengo hilo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana; namshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu yake, lakini kwa kuwa Mheshimiwa Rais alishatoa ahadi wakati wa kampeni mwaka 2020 na Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza kwamba ni mradi wa kimkakati.

Je, kwa kuwa ilikuwa ni ahadi ya Rais, Serikali inatoa tamko gani kuhusiana na jambo hili? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fatma Toufiq, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi stendi ya Chema ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na ahadi zote za viongozi zinatekelezwa kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na mipango inavyoandaliwa. Na katika jibu langu la msingi nimewaelekeza Halmashauri ya Chemba waandae andiko rasmi ambalo litawezesha sasa Serikali kuanza kutoa fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo wa kimkakati, lakini pia ambao pia ni ahadi ya viongozi wetu wa Kitaifa.

Kwa hiyo, niombe watekeleze utaratibu huo na Serikali iweze kuona namna ya kuanza kutekeleza mradi huu. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Bunda ni Halmashauri inayokua lakini pia ina route nyingi za usafiri ikiwepo kwenda Arusha, Mwanza na maeneo mengine, lakini stendi yake ni mbaya sana.

Ni lini sasa Serikali mtatusaidia hasa Halmashauri yetu changa kutujengea stendi ya kisasa na hasa ukizingatia Mji wa Bunda unakua? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Bunda ni Mji ambao unakua, una muingiliano mkubwa wa kibiashara, lakini pia una muingiliano wa magari yanayokwenda katika Mikoa mbalimbali, kwa hiyo, una kila sifa ya kupata stendi ya kisasa na mimi nichukue nafasi hii kwanza kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalitambua hilo, lakini Serikali inalitambua hilo lakini Serikali ya Halmashauri kwa maana ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Halmashauri ya Bunda waanzishe utaratibu wa kufanya tathmini ya gharama ambazo zinahitajika kujenga stendi ile ili wawasilishe Serikalini na sisi tutafanya tathmini na kuona uwezekano wa kupata fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi ya Bunda. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo. Awali ya yote naishukuru Serikali kwa kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Maswali yangu madogo ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kata ya Ikola wamefanya kazi nzuri ya ujenzi wa Hospitali Teule: Nini kauli ya Serikali katika kuwaunga mkono wananchi hawa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Awamu ya tatu na ya nne kwa maana ya upelekaji vifaatiba katika vituo vya afya, tunacho Kituo cha Afya cha Ilembo, kwa bahati mbaya hakikubahatika kupata fedha hizo: Nini kauli ya Serikali katika kupeleka vifaatiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru sana kwa kupongeza juhudi za Serikali za kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivi vya afya, lakini hizi kazi zote zinazofanywa ni dhamira ya Serikali hii ya Awamu ya Sita na Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya kule walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Ikona ambayo wananchi wamechangia nguvu zao kujenga kituo cha afya, kwanza niwapongeze sana kwa kuchangia nguvu zao, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge pia kwa kuhamasisha wananchi hawa, lakini nimhakikishie kwamba Serikali inaendelea na mipango yake ya kuchangia nguvu za wananchi kwa kupeleka fedha ili kukamilisha vituo vya afya ambavyo tayari wananchi wameanza na ujenzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, hii itawekwa kwenye mipango na kadri ambavyo tutapata fedha tutakwenda kuhakikisha kwamba kituo hiki pia kinasaidiwa ili kikamilike na kuanza kutoa huduma bora za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Ilembo nayo kuhusiana na vifaatiba, tumeweka mkakati na katika mwaka huu wa fedha tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 100 zinazotokana na tozo kwa ajili ya vifaatiba katika vituo vyetu. Kwa hiyo, tutaenda kuhakikisha vituo kama hivi pia vinapata fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutampa kipaumbele katika kituo hicho. Ahsante sana.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, moja ya kazi ya Serikali ya ujenzi wa vituo vya afya vilevile ni kupandisha hadhi vituo vya afya kuwa Hospitali za Wilaya. Hospitali ya Manyamanyama ni hitaji la Halmashauri ya Bunda kuwa Hospitali ya Wilaya. Hili swali nimeuliza huu ni mwaka wa 11; na liliamuliwa tangu enzi ya Mheshimiwa Mama Anna Abdallah, Mheshimiwa Mwakyusa, mpaka leo wameweka kibao cha Hospitali ya Wilaya, lakini vifaatiba na madawa mnatoa mgao wa kituo cha afya:-

Mheshimiwa Spika, ni lini sasa Serikali hii itaipa Hospitali ya Manyamanyama mgao wa vifaatiba na madawa kama Hospitali ya Wilaya na siyo tena kituo cha afya, maana kinatoa huduma mpaka katika Wilaya za jirani? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kupandisha vituo vya afya kuwa hospitali una vigezo kadhaa ambavyo vimewekwa. Moja ni kuwa na Halmashauri ambayo haina Hospitali ya Wilaya ndipo kituo kimojawapo cha afya ambacho kinakidhi sifa, kinapandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Halmashauri. Kwa mfumo, sera na miongozo ya sasa,

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Wilaya ipo moja tu katika Halmashauri. Kwa hiyo, kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Bunda ina Hospitali ya Halmashauri; na hiki kituo cha afya kwa nature yake kinahudumia wananchi wengi, tutahakikisha tunaongeza mgao wa dawa na vifaatiba ili iweze kuendana na idadi ya wananchi wanaopata huduma pale wakati tunaendelea kuboresha Hospitali hii ya Wilaya iliyopo katika Halmashauri ya Bunda. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali lakini nilikuwa napenda kumuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Makete ya mwaka 2014 na Makete ya sasa ni ya tofauti sana. Kutokana na utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama Cha Mapinduzi imejengwa lami ambayo imefika hadi Makete, na kwa hiyo mabasi kutoka Dar es salaam na mikoa mingine tayari yameshaanza kuingia Makete.

Je, Serikali ipo tayari kutupatia fedha kutoka kwenye mpango wa miradi ya kimkakati ili Makete ipate kituo cha mabasi kizuri ambacho kinaendana na uhitaji mkubwa wa sasa ambao tunao?

Mheshimiwa Spika, jambo la pili; nakuomba Mheshimiwa Naibu Waziri baada ya Bunge hili kama utakuwa tayari twende Makete kwa ajili ya kuangalia ukubwa wa uhitaji wa kituo cha mabasi pale ndani ya Wilaya ya Makete. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nianze kumpongeza sana Mheshimiwa Festo Richard Sanga kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kuwatetea wananchi wa Jimbo la Makete katika miradi mbalimbali ya kiuchumi pamoja na ya kijamii.

Mheshimiwa Spika, pili, nimhakikishie kwamba Serikali inatambua kwamba baada ya utekelezaji mzuri wa Ilani na barabara ya lami kutoka Njombe kwenda Makete, ambayo pia itatoka Makete kwenda Mbeya Mji wa Makete utafunguka na una kila sababu ya kupata stendi ya kisasa ya mabasi. Ndiyo maana katika katika jibu la msingi, na ninaomba niendelee kusisitiza, kwamba tunawashauri Halmashauri ya Makete, waandae andiko la kimkakati la ujenzi wa stendi ya mabasi ya kisasa ambalo litaonesha business plan yake na uwezo wa kulipa fedha zile ili tuweze kutafuta vyanzo vya fedha, iwe Serikalini au kwa wadau mbalimbali, lakini pia na mapato ya ndani ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, tatu; nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili. Naomba tukae ili tupange ratiba yetu tufike pale; pamoja na mambo mengine tuangalie ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi. Ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa hii.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa uhitaji wa stendi kuu ya mabasi uliopo kule Makete unafanana kabisa na uhitaji wa Stendi ya Mabasi ya Bukoba Mjini. Ningependa kupata kauli ya Serikali; je, sisi Bukoba Mjini tutapata lini stendi mpya ya mabasi hususan ukizingatia kwamba Wilaya ya Bukoba Mjini ndiyo reception ya Mkoa wetu wa Kagera na inaunganisha Kagera na nchi ambazo tunapakana nazo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Stendi ya Mabasi ya Mji wa Bukoba ni miongoni mwa stendi ambazo Serikali imeziwekea kipaumbele cha kutosha kwa kuhakikisha kwamba kinatafutiwa fedha; lakini pia nitaangalia kwenye miradi ile ya kimkakati ya TACTIC kama Halmashauri ya Mji wa Bukoba imo ili tuweze kujiridhisha kwamba stendi ile itakuwa sehemu ya ule mradi ambao utakwenda kuhudumiwa.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Lugangira, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Steven Byabato, Naibu Waziri wa Nishati na Mbunge wa Bukoba Mjini kwa kazi kubwa ya kufuatilia stendi hii na mambo mengine; na kwamba nimhakikishie, sisi kama Serikali tutashirikiana nao Waheshimiwa Wabunge wote kutekeleza miradi hiyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kituo cha Afya cha Mlola ndiyo kituo pekee kinachohudumia zaidi ya kata nane lakini kiuo kwa muda mrefu hakina gari la wagonjwa.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kuwapatia Kituo cha Afya Mlola gari la wagonjwa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, vituo hivi vya Gare na Ngwelo ni vituo vilivyojengwa na nguvu za wananchi kwa muda mrefu sana. Vituo hivi nilianza kuviongelea tangu 2017, 2018, 2019, 2020 mpaka sasa hivi 2021 lakini hakuna majibu ya kuridhisha, majibu ni haya ya nadharia bila vitendo. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari sasa kuongozana nami ili akaone kazi iliyofanywa na wananchi wale? Nadhani hapo ndipo atatupa fedha za kujenga vituo vile.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani O. Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Mlola kinahudumia wananchi wengi, kata nane katika Jimbo lile la Lushoto na ni kituo muhimu sana kuhakikisha kwamba kinapata gari la wagonjwa ili kiweze kufanikisha rufaa lakini pia na huduma dharura kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Lushoto. Naomba nimhakikishe Mheshimiwa Shekilindi kwamba Serikali inatambua kwamba kituo hicho kinahitaji kuwa na gari la wagonjwa na taratibu za kupata magari ya wagonjwa katika kituo hicho lakini pia katika Vituo vingine vya Afya zinaendelea kufanyika na tutaendelea kupelekea magari hayo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tumelichukua na tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na Vituo vya Afya vya Gare na Ngwelo kuanza kujengwa kwa nguvu za wananchi kwa muda mrefu, kwanza, Serikali inawapongeza sana wananchi wa Lushoto kwa kujitolea kuchangia kuanza ujenzi wa Vituo hivi vya Afya. Serikali inatambua sana mchango wa wananchi na itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kuunga mkono nguvu za wananchi katika kukamilisha vituo hivi vya afya. Naomba nimhakikishie, pamoja na kwamba vituo hivi kwa muda mrefu vimekuwa vikiahidiwa kupatiwa fedha, jitihada zinaendelea kuendelea kutafuta fedha na mara zitakapopatikana Vituo hivi vya Afya vitapewa kipaumbele.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Changamoto zilizopo Jimbo la Lushoto zinafanana kabisa na zilizopo Jimbo la Meatu kwa kuwa ni Kituo cha Mwanhuzi pekee kilichoongezewa miundombinu ambacho pia kinatumika kama Hospitali ya Wilaya.

Je, Serikali haioni haja ya kuongeza miundombinu katika Kituo cha Afya Bukundi ili kukabiliana na wagonjwa ambao pia wanachangizwa na wagonjwa kutoka Wilaya ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Bukundi katika Jimbo la Meatu ni muhimu sana na kwa bahati njema nakifahamu vizuri nikiwa nimefanya kazi huko kama Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu. Nafahamu kwamba tunahitaji kukiboresha na kukitanua kituo kile ili kiweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi kwa sababu kipo pembezoni sana na eneo lile kuna umbali mkubwa sana kufika kwenye vituo vingine vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge Leah Komanya kwamba Serikali inatambua umuhimu huo na mipango inaendelea kufanywa kutafuta fedha. Mara fedha zikishapatikana tutahakikisha kituo hicho ni miongoni mwa vituo ambavyo majengo yake yatakwenda kupanuliwa ili kiweze kutoa huduma bora zaidi za afya.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa suala hili linafanana kabisa na Vituo vyangu vya Kisesa na Nyanguge, ni vituo vya siku nyingi ambavyo havitoi huduma inayostahili kwa wananchi.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha hasa kufanya ukarabati na kuvipatia vifaa vya kutolea tiba katika Vituo vya Nyanguge na Kisesa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniventura Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kusema kwamba sisi sote Waheshimiwa Wabunge tunafahamu kazi kubwa sana ambayo imefanywa na ambayo inaendelea kufanywa na Serikali yetu katika kuhakikisha kwanza tunajenga vituo vya afya lakini tunakarabati vituo vya afya. Sisi sote ni mashahidi kwa kipindi hiki cha miaka mitano jumla vituo vya afya vipatavyo 487 vimeendelea kujengwa na kukarabatiwa na vimeanza kutoa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hatua moja inatupelekea kuendelea na hatua nyingine. Naomba nimhakikishe Mheshimiwa Kiswaga, kwanza kuhusiana na Kituo cha Afya cha Kisesa na Nyanguge kwamba vinahitaji ukarabati, ni kweli na suala ambalo tunakwenda kulifanya ni kuanza kuweka taratibu za ukarabati na upanuzi wa vituo hivi kadri ya upatikanaji wa fedha. Tuna kata nyingi, tutakwenda kwa awamu, si rahisi kumaliza vituo vyote kwa pamoja lakini vituo hivi vyote ni kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na vifaatiba, naomba niwakumbushe watendaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa, maelekezo yalikwishatolewa Serikali imekuwa ikigharamia ujenzi wa vituo hivyo, kuanzia hospitali za halmashauri, vituo vya afya na zahanati. Katika hospitali za Halmshauri tumetenga bajeti kwa ajili ya vifaa tiba lakini katika vituo vya afya, tumewaelekeza Wakurugenzi katika mamlaka za Serikali za Mitaa kutenga fedha ili tuweze kununua vifaatiba.

Kwa hiyo, ni muhimu sana Mamlaka ya Halmashauri ya Magu wahakikishe wanatenga fedha katika mapato ya ndani na fedha zipatikanazo na malipo ya cost sharing ili kununua vifaatiba. Kwa ujumla, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuboresha miundombinu hii kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, napenda nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu hayo, lakini ujenzi wa stendi hii ulitakiwa uanze toka mwaka 2010/2011 ambapo Serikali iliweza kuzuia maeneo ya wananchi wa Kata za Moshono na Kata za Olasiti na maeneo hayo yaliwekwa mpaka kwenye master plan ya Jiji la Arusha. Sasa hivi Serikali imefanya maamuzi ya kwenda kujenga stendi kwenye eneo lingine la Bondeni City.

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yangu ya nyongeza, napenda kufahamu kwanza, je, sasa Serikali ina mpango gani na yale maeneo ya Olasiti na Moshono ambayo yalitengwa maalum kwa ajili ya kujenga stendi na yameishingia kwenye master plan? Je, Serikali sasa hivi inawaruhusu wananchi wale waende wakayaendeleze maeneo yao? Je, wako tayari kupabilisha master plan au Serikali inao mpango wa kulipa fidia?

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho wa siku wananchi wale walitarajia kwamba Serikali ingeweka shughuli yoyote ya kiuchumi pale, hata kama sio stendi, pengine soko au shughuli yoyote, ingesaidia shughuli za kiuchumi za watu wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mrisho Gambo ushauliza maswali matatu tayari katika swali lako la kwanza la nyongeza na maswali yanayoruhusiwa ni mawili. Mheshimiwa Naibu Waziri, majibu.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunielewa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa dhamira ile ya kuhakikisha inaboresha miundombinu ya vitega uchumi kwa maana ya miradi ya kimkakati katika Jiji la Arusha, ilitenga maeneo haya na mradi huu ulitarajiwa kuanza mwaka 2010/2011. Yale maeneo ambayo yalitengwa awali, ni yale ambayo wananchi waliahidiwa kwamba watafidiwa lakini pia ili kitega uchumi kiweze kujengwa eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sababu kadhaa ambazo zilifanya Halmashauri ya Jiji la Arusha lakini na Serikali kuona ni vema sasa eneo la Bondeni City ambalo ni kubwa na linaweza likasaidia zaidi kwa maana ya geographical location yake kuwa na stendi ya kisasa ambayo itasaidia zaidi kuboresa mapato lakini pia huduma kwa wananchi wa Arusha. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo kwamba nalichukua jambo hili twende tukalifanyie tathmini zaidi, tuweze kuona sababu ambazo zimetupelekea kuhamisha kwenda sehemu nyingine lakini tuweze kuona nini kitafanyika sasa katika lile eneo ambalo mara ya kwanza lilikuwa limedhamiriwa kujenga stendi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sehemu ya pili naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama nilivyotangulia kusema Serikali inadhamiria kujenga miradi hii ya kimkakati yakiwemo haya masoko kisasa. Kwanza kuboresha huduma kwa wananchi, lakini pili kuwezesha halmshauri kupata mapato katika vyanzo vyake vya ndani. Baada ya tathmini hiyo na baada ya kumpata Mkandarasi Mshauri tutahakikisha kwamba tunakwenda kuanza ujenzi wa soko hilo la kisasa katika Jiji la Arusha.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, mazingira ya swali Arusha yanahusika kabisa na Mkoa mpya wa Songwe, yanafanana vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa katika Mkoa wa Songwe, kuna eneo ambalo lilikuwa limetengwa la Mbimba TaCRI kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya Mkoa. Kwa kuwa michoro tayari ilishakamilika kwa muda mrefu karibu zaidi ya miaka sasa mitatu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba stendi kubwa ya Mkoa wa Songwe inaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Songwe tunahitaji kujenga Stendi ya Kisasa ya Mabasi. Katika majibu yangu ya msingi, nimeeleza kwamba tunatarajia kujenga stendi katika maeneo haya yote ambayo tayari yamekwishatambuliwa na sasa tunaendelea kufanya mazungumzo na Benki ya Dunia ili kupata fedha kwa ajili ya kuwezesha sasa ujenzi wa maeneo haya ya miradi ya kimkakati kuanza. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Hasunga kwamba katika miradi hiyo inayokuja, mara mazungumzo yatakapokamilika na fedha hizo kupatikana basi tutaweka kipambele pia katika kuwezesha Kituo cha Mabasi cha Mkoa wa Songwe kuanza kujengwa.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa changamoto za stendi katika Jimbo la Arusha Mjini, zinafana sana na changamoto za kukosekana stendi katika Jimbo la Busokelo. Je, ni lini Serikali itajenga stendi za Miji ya Ruangwa, Ruangwa Mjini pamoja na Kandete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Atupele Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali inatambua uhitaji wa masoko ya kisasa katika Kata hizo ambazo Mheshimiwa Atupele Mwakibete amezitaja, lakini pia katika maeneo mengine kote Nchini. Naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba dhamira hiyo ya Serikali bado ipo na mipango ya kutafuta fedha kwa ajili ya kuwezesha ujenzi wa masoko hayo ya kisasa inaendelea. Mara fedha hizo zitakapopatikana tutahakikisha tunatoa vipaumbele katika maeneo hayo ambayo tayari yamekwishatambuliwa ili tuweze kuwekeza miradi hiyo ya kimkakati na kuwezesha huduma kuendelea. Kwa hiyo, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mwakibete kwamba maeneo hayo pia tutayapa kipaumbele mara fedha zikipatikana ili ujenzi wa masoko hayo uweze kuanza.
MHE. VINCENT P. MBOGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri. Ukanda wa Ziwa Tanganyika akina mama wengi wanakufa kwa kutokupata huduma za afya, hasa upande wa ambulance boat kwa sababu kule miundombinu ya barabara hakuna, usafiri wao ni ndani ya maji na vijiji vipo vingi sana ndani ya Ziwa Tanganyika ambavyo vinatumia usafiri wa boti. Ni lini Serikali itapeleka ambulance boat kwa ajili ya kuokoa akina mama wajawazito? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika mwambao ule wa Ziwa Tanganyika kuna changamoto ya usafiri pale ambapo tunapata dharura za wagonjwa na hususan akina mama wajawazito ambao wanahitaji kwenda kwenye vituo vya rufaa kwa ajili ya huduma za upasuaji. Serikali imeendelea kuweka mipango ya kuhakikisha kwamba maeneo hayo ambayo yana changamoto kubwa za usafiri, hasa ambulance kwa maana ya ambulance boats, tunaendelea kuangalia utaratibu mzuri zaidi wa kutenga fedha kadri zitakavyokuwa zinapatikana ili tuwezeshe ufanisi wa rufaa katika maeneo hayo ili tuendelee kuokoa maisha ya wananchi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo kwamba suala hili kama Serikali tunalichukua, tutalifanyia kazi na kuona namna bora zaidi ya kupata ambulance boat ili iweze kusaidia wananchi katika Jimbo la Nkasi Kusini. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Makete, hasa Kata za Ipepo na Ikuo, wana changamoto pia ya kituo cha afya. Kwa Ikuo wana majengo tayari wameshajenga kwa nguvu za wananchi lakini bado Serikali haijamalizia na Ipepo tayari wameshaandaa tofali kwa ajili ya kujenga kituo cha afya. Je, ni lini Serikali itaongeza nguvu kuhakikisha kwamba majengo haya yanakamilika kwa ajili ya wananchi wangu wa Ipepo na Ikuo, hasa ikizingatiwa kwamba wana zaidi ya kilometa 20 kwenda kufuata huduma za afya na tayari wameshaonesha jitihada za kuweka nguvukazi hizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba majibu ya Serikali kwa ajili ya wananchi wangu hao.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuwapongeza wananchi wa Kata za Ipepo na Ikuo katika Jimbo la Makete kwa kuonesha nguvu kubwa ya kuwekeza katika ujenzi wa vituo vya afya na hatua nzuri ambayo wameifikia. Serikali imeendelea kusisitiza wananchi kuchangia nguvu zao kuanza ujenzi wa miradi ya vituo vya afya na zahanati na Serikali kuchangia nguvu za wananchi katika umaliziaji wa vituo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Festo Sanga kwamba katika mwaka ujao wa fedha, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuchangia nguvu za wananchi katika ukamilishaji wa maboma. Nimhakikishie kwamba katika maeneo ambayo tutawapa kipaumbele ni pamoja na Kata hizi za Ipepo na Ikuo ili wananchi waweze kupata nguvu ya Serikali kukamilisha vituo hivyo vya afya.
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyo kwa Jimbo la Nkasi Kusini, hali ni hiyohiyo ama mbaya zaidi kwa Halmashauri ya Wilaya ya Muheza ambapo tuna kata 37 na vituo viwili tu vya afya. Sasa swali langu, Serikali ina mpango wowote wa kuongeza vituo vya afya Wilayani Muheza ili kusogeza huduma za afya karibu na wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamis Mwinjuma, Mbunge wa Muheza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Jimbo la Muheza lina kata 37 na vituo vya afya viwili tu na hali hii ipo katika karibu majimbo yote nchini. Tunafahamu tuna kata zaidi ya 3,900 na ndiyo maana Serikali imeweka mpango wa kujenga vituo vya afya kwa awamu. Ni kweli kwamba hatuwezi kukamilisha kujenga vituo katika kata zote ndani ya mwaka mmoja wa fedha, lakini Serikali imedhamiria na inatambua kwamba tuna kazi ya kufanya kwa awamu kwa kadri ya fedha zinavyopatikana na kuendelea kujenga vituo vya afya katika kata zetu na kujenga zahanati katika vijiji na hospitali za halmashauri katika ngazi za halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mwinjuma kwamba katika mipango ya Serikali inayokuja, tutaendelea kuomba kuidhinishiwa fedha kwa ajili ya kuendelea kujenga vituo vya afya katika kata nchini kote zikiwemo kata katika katika Jimbo hili la Muheza.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Changamoto iliyopo Nkasi ndiyo changamoto iliyopo Kyerwa. Kyerwa tuna kata 24 lakini vituo vya afya vinavyotoa huduma ni viwili na kipo Kituo cha Afya Nkwenda ambacho jengo la mama na mtoto halijakamilika. Lini Serikali itakamilisha kituo hiki ili kiweze kutoa huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Innocent Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kutoa ufafanuzi, kwamba dhamira na malengo ya Serikali na katika mipango yote ambayo Serikali inaandaa, ni pamoja na kuhakikisha inachangia nguvu za wananchi katika kukamilisha maboma ya zahanati, vituo vya afya na kupanua hospitali za halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo hili la Kyerwa ambapo kuna vituo vya afya viwili na Kituo cha Afya cha Nkwenda ambacho kimeshajengewa jengo la RCH na halijakamilika, ni miongoni mwa vituo ambavyo vitaendelea kupewa kipaumbele katika bajeti za Serikali ili viweze kukamilishwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba katika mwaka ujao wa fedha, Mheshimiwa Waziri akija kuwasilisha bajeti hapa, tuna vituo takribani 121 ambavyo tunatarajia kwenda kujenga kwa fedha za Serikali Kuu na fedha za mapato ya ndani ya halmashauri. Kwa hiyo kwa kupitia mpango huo tutaendelea kusogeza zaidi huduma ikiwemo katika Jimbo hili la Kyerwa.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwanza, naomba niipongeze Serikali kwa kuongeza bajeti ya madawa na vifaa tiba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Kituo cha Afya cha Mwabayanda jengo la kuhifadhi maiti liko tayari lakini halina friji, je, ni lini Serikali itapeleka friji ya kuhifadhia maiti? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hospitali na vituo vya afya vya Mkoa wa Simiyu tuna upungufu wa madawa; je, Serikali imejipangaje kutupelekea madawa za kutosha kwenye hospitali na vituo vyetu vya afya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napokea pongezi zake kwa Serikali kwamba imetenga fedha kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na shilingi bilioni 30 mwaka 2015 mpaka takribani shilingi bilioni 270, karibu mara tisa ndani ya miaka hii mitano. Hiyo ni dalili kwamba Serikali inathamini na imedhamiria kuhakikisha inaboresha upatikanaji wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba katika vituo vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu jengo la mortuary kukamilika na kuhitaji jokofu, naomba nimueleze Mheshimiwa Mbunge Esther Lukago Midimu kwamba Serikali inapeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya huduma kama ambavyo tulifanya katika Kituo hiki cha Mwabayanda. Pia tumeelekeza watendaji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa baada ya Serikali kupeleka fedha katika vituo hivyo na kukamilisha miundombinu, ni wajibu wao pia kupeleka sehemu ya fedha za maendeleo, ile asilimia 40 au 60 kwa ajili ya kununua baadhi ya vifaa tiba ili kuboresha huduma katika jamii zao. Kwa hiyo, ni muhimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Maswa aone namna bora pia ya kutenga fedha za kununua jokofu kwa ajili ya chumba cha kuhifadhia maiti katika jengo lile la Kituo cha Afya cha Mwabayanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na upungufu wa dawa; Serikali imeendelea kuboresha sana upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu kutoka asilimia 65 mwaka 2015 mpaka takribani asilimia 90-94 katika mwaka huu wa fedha. Lengo la Serikali, kwanza ni kuendelea kuboresha upatikanaji wa dawa kwa kuboresha makusanyo ya fedha za uchangiaji wa huduma za afya katika vituo vyetu. Pili ni kuendelea kupeleka fedha Bohari Kuu ya Dawa ili kuendelea kupata dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa kwenye vituo vya afya katika Mkoa wa Simiyu na nchini kote.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, matatizo ya dawa yanayojitokeza katika zahanati zetu ni sawa na yanayojitokeza katika Zahanati za Ipinda, Kyela na hata pale mijini. Ni mpaka lini tutasubiri tatizo hili liishe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Mlaghila Jumbe, Mbunge wa Kyela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha; kwanza bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba lakini pili, imeendelea kuboresha sana upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vyetu. Ni kweli pamoja na maboresho haya bado kuna changamoto ya upatikanaji wa dawa katika baadhi ya vituo na halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ambayo Serikali tumeyatoa, kwanza ni kuhakikisha watendaji katika Mamlaka za Serikali za Mitaa wanatumia vizuri fedha zitokanazo na uchangiaji wa huduma za afya kwa maana ya cost sharing. Tumejifunza kwamba baadhi ya halmashauri hazitumii vizuri fedha za cost sharing na tumewapa maelekezo kuhakikisha angalau asilimia 50 hadi 60 ya fedha za uchangiaji zinakwenda kununua dawa, vitendanishi na vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika swali la msingi, Serikali imeendelea kuongeza bajeti na itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa kwa kuongeza bajeti na kusimamia matumizi bora ya dawa katika vituo vyetu. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kulifanyia kazi suala hilo. Pia niwaombe Waheshimiwa Wabunge, kwa sababu sisi ni Madiwani katika mabaraza yetu kufuatilia kwa karibu matumizi ya dawa katika vituo vyetu na kuendelea kushirikiana na Serikali kuhakikisha makusanyo yanakuwa bora zaidi.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Kishapu na wananchi wa Kishapu kwa ujumla wameweza kujenga health centers tatu; Health Center za Dulisi, Mwigumbi na Mwang’halanga. Hata hivyo, health centers hizi zina upungufu mkubwa wa dawa na vifaa tiba lakini pia lipo tatizo la upungufu mkubwa wa wafanyakazi (watumishi). Je, Serikali inasema nini kuhusiana na suala zima la kutatua tatizo hili katika Wilaya ya Kishapu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza wananchi wa Jimbo la Kishapu kwa kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa vituo vya afya vitatu, lakini kwa kuhakikisha kwamba vituo hivyo vinaanza kutoa huduma ili kuweza kuboresha huduma za afya katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika swali la msingi, lakini katika maswali ya nyongeza yaliyofuata ni kwamba hali ya upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu imeendelea kuimarika. Hata hivyo, tunafahamu bado kuna changamoto katika maeneo mbalimbali ikiwemo katika kata hizi ambazo zipo katika Jimbo la Kishapu.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la muhimu ambalo Serikali inaendelea kulitekeleza; moja, ni kuhakikisha tunaendelea kupeleka dawa katika vituo hivyo kutoka Bohari Kuu ya Dawa kwa wakati na kuendelea kuboresha bajeti ya dawa katika vituo hivyo kwa kutumia fedha za mapato ya ndani na fedha zinazotoka Serikali Kuu. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Boniphace Butondo kwamba tutaendelea kushirikiana kwa karibu sana kuhakikisha vituo hivi vinapata dawa na vitendanishi vya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba baada ya ujenzi wa vituo vingi vya afya, automatically tunakuwa na upungufu wa watumishi. Hiyo ni hatua moja. Serikali imeanza na hatua ya ujenzi wa Vituo vya Afya, nasi sote ni mashahidi, tumejenga vituo vingi kwa wakati mmoja, lakini tunaendelea na hatua ya pili ya kuajiri watumishi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuomba kibali cha ajira na kadri watumishi watakavyopatikana, tutahakikisha tunawapeleka katika Vituo hivi vya Afya katika Jimbo la Kishapu na pia katika majimbo mengine kote nchini. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza naipongeza Serikali kwa kutenga fedha kwa ajili ya kutujengea Hospitali ya Nyang’wale ambayo imekamilika kwa asilimia 90; lakini majengo hayo ambayo yamekamilika, anayatumia Mkurugenzi kama Ofisi zake na jengo la Halmashauri lipo kwenye asilimia 34:

Je, Serikali ipo tayari kuongeza fedha ili kukamilisha jengo la Halmashauri ili Mkurugenzi aweze kuhama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Nyang’wale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, majengo haya ya Hospitali za Halmashauri ambayo yamekamilika kwa asilimia 90 na kuendelea, maelekezo ya Serikali ni kuhakikisha majengo yale yanaanza kutoa huduma za awali za afya katika Hospitali hizo za Halmashauri. Ndiyo maana katika hospitali zote 67 za awamu ya kwanza tayari huduma za awali za OPD zinatolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuelekeza kwamba Mamlaka za Serikali za Mitaa katika Wilaya ya Nyang’wale ifanye utaratibu wa kuhakikisha huduma za afya katika hospitali hii iliyokamilika kwa asilimia 90 kwa wananchi, angalau kwa kuanza na huduma za OPD. Pili, Serikali katika mpango wa bajeti wa mwaka ujao itatenga zaidi ya shilingi bilioni 34 kwa ajili ya kukamilisha Hospitali zote za Halmashauri 67 ambazo zilianza ujenzi mwaka 2018/2019 ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Nyangh’wale.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nawapongeza kwa jinsi ambavyo wameweza kutujengea vituo vya afya viwili; cha Buza pamoja na Malawi na vyote vimemalizika katika Halmashauri yetu ya Temeke. Sasa nauliza:-

Je, vifaa tiba vitaingia lini; kwa sababu sasa ni muda mrefu hatujapata vifaa hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba vituo vya afya vikiwemo vya Halmashauri ya Manispaa ya Temeke vimekamilika na kuna changamoto ya vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha ujao tutakwenda kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha vituo hivi vya afya vinapelekewa vifaa tiba. Katika swali langu la msingi nimesema, katika mwaka huu wa fedha jumla ya shilingi bilioni 26 zimeshatolewa tayari; na shilingi bilioni 15 vifaa tiba vimeshapelekwa kwenye vituo vya afya vilivyojengwa kwenye awamu ya kwanza na ya pili; na shilingi bilioni 11 zipo katika hatua za manunuzi kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba katika vituo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Vituo vya Afya hivi vya Temeke vilijengwa awamu ya tatu na awamu ya nne, kwa hiyo, vitakuwa katika mpango wa bajeti wa mwaka 2021/ 2022. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo litaendelea kufanyiwa kazi. (Makofi)
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na Sera ya Matibabu Bure kuendelea kutekelezeka, lakini bado kuna wazee wengi hawajapatiwa vitambulisho hivyo vya kuwawezesha kupata matibabu hayo:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wazee wote wenye sifa wanapata vitambulisho hivyo ili waweze kunufaika na Sera ya Matibabu Bure? (Makofi)

(b) Kuna malalamiko hata kwa wale wazee wachache wenye vitambulisho hivyo; wanapofika hospitalini wanaambiwa hakuna dawa: Je, ni lini Serikali itahakikisha ukosefu wa madawa huu unakwisha ili kuwaondolea wazee wetu kero hiyo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Sera ya Wazee inatambua kwamba tunahitaji kuainisha wazee wote wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo ili waweze kupata matibabu bila malipo. Serikali imeendelea kuweka utaratibu kupitia Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kupitia Maafisa Ustawi wa Jamii na Maafisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauti zetu kupita katika vijiji kwa kushirikiana na Watendaji katika Vijiji na Kata kuwatambua wazee hao wenye sifa, lakini pia kuhakikisha wanapata vitambulisho kwa ajili ya matibabu bila malipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba bado hatujafikia asilimia 100 kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi, lakini jiitihada za kuhakikisha tunafikia hapo zinaendea. Naomba nichukue nafasi hii kuwaelekeza Watendaji Wakurugenzi wa Mamlaka ya Serikali Mitaa wote kote nchi kuhakikisha wanaweka mpango kazi wa kuwatambua wazee wote wenye umri wa miaka 60 na kuendelea, wasio na uwezo na kuweka mipango ya kuwapatia vitambulisho ili waweze kupata matibabu bila malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili ni endelevu, haliwezi kwisha kwa sababu kila siku kuna mtu anafikisha miaka 60. Kwa hiyo, hatuwezi kusema tumemaliza wazee wote, kwa sababu ni suala endelevu, kila mwaka kuna watu ambao wata-turn miaka 60 na Serikali itaendelea kuwatafutia vitambulisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika vituo vyetu kumekuwa kuna malalamiko kwa baadhi ya vituo na baadhi ya Halmashauri kwamba wazee wetu wakifika kwa ajili ya matibabu pamoja na vitambulisho vyao, wanakosa baadhi ya dawa muhimu. Kuna sababu mbili; sababu ya kwanza ni kwamba magonjwa mengi ambayo yanawapata wazee wa miaka 60 na kuendelea mara nyingi baadhi ya dawa zao hazipatikani katika ngazi ya vituo. Kwa hiyo, mara nyingine kunakuwa na changamoto ya magonjwa yale kwa ajili ya advanced cases, lakini wanahitaji kupata labda kwenye ngazi ya wilaya na ngazi ya rufaa, wakienda kwenye vituo vyetu mara nyingine hawapati zile dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeweka utaratibu wa kuendelea kwanza kuwaelimisha wananchi hao, lakini pia kuweka utaratibu wa kuona namna gani zile dawa muhimu katika maeneo husika zitapatikana ili kuwarahisishia wazee wetu kupata matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu ya pili ni ile ambayo nimeelezea kwa ujumla wake kwamba Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba katika vituo vyetu kote nchini ili kuhakikisha wazee wetu na wananchi kwa ujumla wanapata dawa kama ambavyo imekusudiwa.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Changamoto iliyopo Mara ya wazee kutokutibiwa bure ipo kwenye Jimbo la Ngara ambapo hata wale wazee waliokuwa na vitambulisho walinyang’anywa walipofika kwenye vituo vya kutolea huduma za afya:-

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kufika kwenye Jimbo la Ngara kushuhudia namna ambavyo Sera ya Matibabu Bure haitekelezwi kwa hao wazee na kutoa muafaka wa namna nzuri ya hao wazee kupata huduma za matibabu bure? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, Sera ya Matibabu Bila Malipo kwa Eazee inahusika katika mamlaka zote nchini kote, ikiwepo Halmashauri ya Ngara. Kwa hiyo, naomba kwanza nipokee taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge kwamba katika Jimbo la Ngara kuna baadhi ya wazee wenye vitambulisho walinyang’anywa. Suala hilo halikubaliki na wala siYo maelekezo ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimwelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri ya Ngara na Mamlaka za Serikali za Mitaa za Ngara kuhakikisha wanalifanyia kazi suala hili mapema. Serikali inaelekeza kutoa vitambulisho vya matibabu kwa wananchi, wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kunyang’anya vitambulisho vile kwa sababu ni kuwanyima haki wazee hao ambao sera inawatambua kwamba wanahitaji kupata vitambulisho hivyo kwa ajili ya matibabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kufuatana na Mheshimiwa Mbunge kwa ajili ya kulitekeleza hilo, lakini kabla sijaenda, lazima Halmashauri ya Ngara itekeleze maelekezo haya ya Serikali kuhakikisha inaendelea kutoa vitambulisho kwa wazee na hakuna ruksa ya kumnyang’anya mzee yeyote kitambulisho kwa ajili ya matibabu. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu tuna machine ya X-Ray tuliletewa toka mwaka 2002. Swali langu ni hili, katika hospitali hiyo hatuna mtaalam wa X-Ray:-

Je, ni lini Serikali italeta mtaalam wa X-Ray katika Wilaya hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu wana mashine ya X-Ray ambayo kwa kipindi kirefu imekosa mtumishi kwa maana ya mtalaam wa X-Ray. Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeendelea kuwasiliana kwa karibu na Wizara ya Afya, lakini pia na Mamlaka za Serikali za Mitaa kuona namna gani tunapata watumishi hawa ili tuweze kupata mtumishi mmoja na kumhamishia katika Halmashauri ya Wilaya ya Meatu. Wataalam hawa bado ni wachache lakini jitihada za Serikali ni kuendelea kuwasomesha ili tuweze kupata wataalam wengi ili waendane na kasi ya ujenzi wa vituo vya afya ambavyo kimsingi vitahitaji kupata watalaam hawa wa X-Ray.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeshalifanyia kazi na tulishaainisha mtumishi kwa ajili ya kumpeleka Meatu na wakati wowote atakwenda kuanza kutoa huduma ya X-Ray katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu. (Makofi)
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii. Pamoja na nia njema ya Serikali yetu kutoa tiba bure kwa wazee wetu, lakini zoezi zima limegubikwa na ukiritimba wa kutoa tiba kwa wazee wetu.

Je, Serikali haioni busara kuoanisha vitambulisho hivi vinavyotolewa kwa wazee na Bima ya Afya ili wazee wetu wapate tiba stahiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niseme, Serikali imeendelea kuhakikisha inapunguza changamoto ambazo Mheshimiwa anaziita ukiritimba wa Matibabu kwa Wazee Bila Malipo na ndiyo maana tumeainisha utaratibu wa kuainisha, kuwatambua wazee wetu na kuwapa vitambulisho. Hiyo ni sehemu ya jitihada ya Serikali kuhakikisha ule ukiritimba unapungua na kuwawezesha wazee wetu kupata matibabu bila malipo na bila changamoto yoyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupokea wazo lake la kuunganisha vitambulisho pamoja na sehemu ya matibabu kwa wazee ili Serikali iweze kulifanyia tathmini na kuona uwezekano wa kufanya hivyo au uwezekano wa kuendelea kuboresha utaratibu uliopo ili tuweze kuboresha huduma.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nilitaka kuongeza kwenye swali la Dkt. Kikoyo kwenye suala la ku-link huduma za matibabu kwa wazee na Bima ya Afya. Jambo moja ambalo lilituchelewesha labda kuleta kwenye Bunge lako Muswada wa Bima ya Afya kwa wote ilikuwa ni kuweka utaratibu kama huo ambao ukishafanya Bima ya Afya ni compulsory, maana yake lazima Serikali ije na utaratibu wa kuona ni jinsi gani Bima za Afya zitapatikana kwa watu hao kama wazee, akina mama wajawazito pamoja na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, swali la Dkt. Kikoyo ni zuri. Pale ambapo Serikali italeta Muswaada wa Bima ya Afya, pia itaweka sasa utaratibu ambao utaondoa hizi changamoto za matibabu bure kwa wazee.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Dkt. Kikoyo kwamba tukimaliza, nadhani tutakuwa tumepata mwarobaini wa tatizo hili. (Makofi)
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Tunatambua kwamba Serikali ina vituo takribani 16 nchi nzima vya kulelea wazee wetu, lakini huduma za afya zinazopatikana ndani ya vituo vile kwa kweli ni kama huduma ya kwanza tu:-

Je, Serikai haioni kuna haja ya kuweka huduma bora ndani ya vituo vya kulelea wazee wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, majengo au nyumba za kulelea wazee wetu zilizopo kote nchini zinaendelea kupewa huduma za muhimu kwa kutumia taasisi mbalimbali ikiwepo Mamlaka ya Serikali za Mitaa ili kuwezesha wazee wetu kuishi katika mazingira bora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la huduma za afya katika maeneo hayo, kumekuwa na utaratibu wa karibu wa uratibu kati ya Maafisa Ustawi wa Jamii na Watoa Huduma katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kufika katika maeneo hayo, lakini pia kuweza kuchunguza afya za wazee wetu na kuwapatia matibabu pale inapobidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu huu tutaendelea kuuimarisha kuona namna gani wataalam katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa wanaweka utaratibu wa mara kwa mara wa kuwatembeala wazee wetu katika maeneo hayo wanayoishi na kutambua wale wenye dalili za kuhitaji matibabu waweze kupata matibabu kwa urahisi zaidi. (Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:- Kwa kuwa barabara za Bugoma kwenda Mchigondo barabara ya Igundu kwenda Bulomba na barabara ya kutoka Mranda kwenda Mwiliruma hazipitiki kabisa kwa muda mrefu.

Je Serikali iko tayari kutengeneza barabara hizo kwa kutumia hata mfuko wa maafa?

Mheshimiwa Spika, kwa vile kuona ni kuamini yaani seeing is believing je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari baada ya kikao hiki tuongozane nae ili akajionee mwenyewe hali ilivyo katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hizi ambazo Mheshimiwa Kajege amezitaja katika Jimbo la Bunda zimeharibika kufuatia mvua nyingi sana ambazo zimeendelea kunyesha kote nchini.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka mpango muhususi wa kwenda kuhakikisha barabara hizi ambazo zimeharibiwa na mvua na hazipitiki zinatengenezwa mapema iwezekanavyo ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kusafirisha lakini na kusafiri katika huduma mbalimbali za kiuchumi, na kijamii. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutahakikisha katika mpango uliopo tunatoa kipaumbele cha hali ya juu katika barabara hizi zilizopo katika Jimbo la Mwibara.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI tuko tayari wakati wowote kushirikiana na Waheshimiwa Wabunge na kufuatana nao katika majimbo hayo ili tuendelee kuwahudumia wananchi. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Kajege kwamba niko tayari baada ya kikao hiki tutapanga tuone ratiba nzuri ya kwenda katika Jimbo lake ili kuendelea kuwahudumia wananchi.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika Ahsante sana kwa kuniona changamoto ya barabara katika Jimbo la Mwibara ni sawasawa kabisa na changamoto za barabara katika Jimbo la Kalenga Mkoani Iringa. Kumekuwa na changamoto kubwa sana na barabara ya kutoka Iringa Mjini kuelekea Kata za Muhota na Magulilwa kutoka Kijiji cha Kitayawa kwenda Nyabula ambako kuna Hospitali ya Misheni ambako wananchi wanatibiwa barabara imekatika kabisa haipitiki imekatika daraja limekatika.

Je! Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wananchi wa jimbo hili la Kalenga hususani wale wale wa…

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, taarifa kidogo.

MHE. GRACE V. TENDEGA: …Kata ya Mpota wanaweza wakapata mahitaji ya barabara.

SPIKA: Taarifa ya nini yuko wapi anayesema taarifa?

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Samahani unjuka ndio unaotusumbua Kiswaga hapa. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Ndio Mheshimiwa Kiswaga!

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Ni unjuka tu unatusumbua lakini kama unaniruhusu nitasema neno moja.
(Kicheko)

SPIKA: Karibu nakuruhusu.

T A A R I F A

MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA, Mheshimiwa Spika, ahsante sana hiyo barabara ya kutoka Kitayao kwenda Nyabula tayari nimeshafanya mpango nimeongea na TARURA na sasa tumeshaweka mabomba hilo daraja linaanza kujengwa hivi karibuni ahsante sana tulipata fedha ya dharula nakushukuru. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Grace Victor Tendega unapokea hiyo taarifa? Halafu tuendelee na swali lako lipi sasa baada ya taarifa hiyo.

MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, kwa uchungu kabisa ninazungumza hapa sipokei taarifa hiyo wananchi wale wanapata shida sana hakuna chochote anachokisema kimefanyika pale barabara imekatika na wananchi awapati huduma kwa hiyo naomba swali langu lijibiwe. (Makofi)

Ni lini Serikali itahakikisha wananchi hawa wanapata huduma ya barabara waweze kupata huduma zingine na matibabu na kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Kiswaga Mbunge wa Jimbo la Kalenga kwa juhudi kubwa sana anazozifanya kuhakikisha wananchi wa Jimbo la Kalenga wanapata barabara bora na hivyo wanaendelea na shughuli za kiuchumi na kijaamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nisema barabara hii ya kutoka Iringa Mjini kwenda Kata ya Maguliwa na maeneo haya kuna hospitali Serikali imeendelea kuhakikisha inatoa kipaumbele kwenye barabara ambazo zinapeleka huduma za jamii kwa wananchi, zikiwemo hospitali, shule na maeneo mengine yenye huduma za kijamii.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotanguliwa kusema tumepata baraka ya mvua mwaka huu, lakini tunafahamu baraka hiyo imeambatana na uharibifu wa baadhi ya madaraja, ma-calvati na barabara zetu. Naomba nimuhakikishie kwamba Serikali inaendelea kuweka mipango ya haraka ikwezekanavyo kuhakikisha barabara ile aliyoisema inakwenda kutengenezwa na hilo daraja lifanyiwa matengenezo ili wananchi waweze kupita na kupata huduma hizo za afya na huduma nyingine. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge jambo hilo linafanyiwa kazi na Serikali.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Jimbo la Tandahimba pamoja na Newala Vijijini lina changamoto ya upatikanji wa vifaatiba pamoja na vitenganishi hali ambayo wakati mwingine inasababisha akinamama wanaojifungua kwenda kutafuta kadi za kliniki mitaani. Je, upi mpango wa dharura wa Serikali wa kunusuru hali hiyo ya upatikanaji wa vifaa tiba pamoja na vitendanishi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Jimbo la Newala Vijijini lenye Kata 22 lina vituo vitatu tu vya kutolea huduma za afya hali ambayo inaleta changamoto kubwa ya upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi wake. Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Jimbo la Newala Vijijini ili wananchi wale wapate huduma za afya kama ambavyo inahitajika? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya utoaji huduma za afya katika vituo vya afya kwanza kwa kutenga fedha kwa ajili ya kununua vifaatiba, vitendanishi lakini pia ununuzi wa dawa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha huu tunaoendelea nao Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 26 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba na tayari shilingi bilioni 15 zimekwishanunua vifaatiba na vimekwishapelekwa kwenye vituo vya afya vya awamu ya kwanza na awamu ya pili. Kiasi cha shilingi bilioni 11 kiko katika hatua za manunuzi na mara moja vifaa hivyo vitanunuliwa na kupelekwa kwenye vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kituo cha afya katika Jimbo la Newala ni moja ya vituo vya afya vilivyojengwa katika awamu ya tatu na ya nne na hivyo vituo hivi vitakwenda kutengewa fedha za ununuzi wa vifaatiba katika mwaka wa fedha 2021/ 2022. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Maimuna Mtanda kwamba vituo vyake hivi vya afya vitawekewa mpango wa kununuliwa vifaatiba ili viendelee kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na idadi ya vitu vya afya katika kata za Jimbo la Newala Vijijini, ni kweli Serikali inatambua kwamba bado kuna uhitaji mkubwa wa vituo vya afya katika kata za Jimbo la Newala Vijijini na nchini kote kwa ujumla na ndiyo maana katika mwaka wa fedha ujao ambapo Mheshimiwa Waziri atawasilisha Bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tunatarajia kuendelea kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya afya katika kata za Jimbo hili la Newala na nchini kote kwa ujumla. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, suala hili litaendelea kufanyiwa kazi.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nina maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali na pesa ambayo tumeipata hiyo shilingi bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa sababu majengo yanaelekea kukamilika na tumefikia mwisho sasa, ni nini mpango wa Serikali kutupatia vifaatiba ili majengo haya angalau yaweze kuanza kufanya kazi haraka iwezekanavyo kwenye robo ya kwanza ya Mwaka wa Fedha 2021/2022?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa sababu hospitali hii bado ni sehemu ya kwanza itakuwa haiwezi kulaza wagonjwa, ni nini mpango wa Serikali kwenye kutupatia ambulance mpya na ya kisasa ili angalau wagonjwa wale ambao hawataweza kupata huduma kwenye Hospitali ya Wilaya waweze kukimbizwa na kupatiwa huduma sehemu nyingine kipindi tunaendelea na kukamilisha ujenzi wa awamu ya pili? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Eng. Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba majengo haya ya Hospitali ya Halmashauri ya Biharamulo yako katika hatua za mwisho za ukamilishaji. Katika mpango wa bajeti wa mwaka 2021/2022, Serikali itatenga fedha kwa ajili ya kwenda kununua vifaatiba kwa ajili ya hospitali hizi mpya ambazo zinaendelea na ujenzi. Kati ya hospitali hizo, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo ni moja ya hospitali ambazo zitatengewa bajeti hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili tunahitaji kuwa na magari ya wagonjwa katika hospitali zetu za halmashauri na mipango ya Serikali inaendelea kufanyika ili kuona namna ambavyo tunaweza tukapata magari hayo na kuyafikisha katika halmashauri hizi. Kwa hivyo, Hospitali ya Halmashauri ya Biharamulo ni moja ya hospitali ambazo zitawekewa mpango wa kupata gari la wagonjwa ili tuweze kuboresha zaidi huduma za afya katika eneo hilo.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru Naibu Waziri wa TAMISEMI kwa majibu mazuri, lakini vile vile niipongeze Serikali kwa kutoa huduma nzuri katika maeneo mbalimbali kwenye fani ya afya. Hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa hospitali hiyo ilijengwa mwaka 1970, jengo la OPD na jengo la upasuaji ni majengo ambayo yamepitwa na wakati na hayaendani na hadhi ya hospitali ya wilaya pamoja na jengo la wodi ya watoto ambao limekosekana kabisa.

Je, Serikali itaanza lini kushughulikia ujenzi wa majengo ya OPD, upasuaji na wodi ya Watoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika hospitali hiyo kuna uhaba wa watendaji, wafanyakazi, Madaktari na watendaji wasaidizi. Je, ni lini Serikali itachukua hatua ya kuhakikisha kwamba changamoto hiyo inatatuliwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas William, Mbunge wa Mbinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee pongezi za Mheshimiwa Mbunda na kwamba Serikali imeendelea kuboresha sana huduma za afya kwa kujenga miundombinu, lakini pia kuhakikisha vifaatiba na dawa zinapatikana. Kuhusiana na hospitali hii kuwa kongwe ni kweli. Hospitali hii imejengwa miaka ya 70 na ni hospitali ambayo kimsingi ni chakavu, inahitaji kuboreshewa miundombinu ili iweze kuendana na majengo ambayo yanaweza kutoa huduma bora za afya kwa ngazi ya hospitali ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na hayo, ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeeleza kwamba Serikali imeanza kufanya tathmini ya uchakavu wa majengo yale na upungufu wa majengo ambayo yanahitajika katika hospitali ile ili sasa tuweze kuona namna ya kutenga fedha kwa ajili ya kuanza either, kukarabati majengo yale na kuongeza yale majengo yanayopungua au kuanza ujenzi wa hospitali mpya. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tathmini hiyo itakapokamilika tutakuja na jawabu la njia sahihi ya kwenda kutekeleza ili kuondokana na changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kuna changamoto ya upungufu wa watumishi katika kada mbalimbali katika hospitali hiyo na nchini kote kwa ujumla. Katika bajeti yetu tumeeleza mipango kwamba baada ya kukamilisha miundombinu ya majengo, tutakwenda kuhakikisha tunaboresha upatikanaji wa vifaatiba, lakini suala linalofuata muhimu na linapewa kipaumbele cha hali ya juu ni kuhakikisha sasa tunakwenda kuomba vibali vya kuajiri watumishi wa afya katika ngazi zote za vituo vya afya, zahanati na hospitali ili tuweze kutoa huduma bora zaidi. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunda kwamba, katika Hospitali hii ya Mji wa Mbinga pia tutaweka kipaumbele katika kuajiri watumishi ili kuendelea kuboresha huduma za afya.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nashukuru.

Niseme tu kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri nirudie kumuomba kama kuna uwezekano angalau wa kufika Rorya kuitambua na kuielewa jiografia ya Rorya ilivyokaa. Nimekuwa nikimuomba hii ni mara ya pili tena narudia kumuomba. Imani yangu akifika atagundua hiki Kituo cha Afya ambacho tumekuwa tukikizungumzia kinahudumia kata zaidi ya tano ikiwemo Kata ya Kyang’ombe, Baraki, Komuge, Kisumwa na Rabol. Inahudumia vijiji zaidi ya 27; population wide ambayo inakwenda kupata huduma pale sio chini ya watu 50,000 kulingana na jiografia ilivyokaa. Umbali wa kutoka kituo hiki cha afya mpaka Hospitali hii ya Wilaya inayojengwa ni zaidi ya kilometa 40 ndiyo maana mara ya kwanza nilikuwa namuomba sana tupate daraja la Mto Moli ili kufupisha safari hii.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu la kwanza la nyongeza; Mheshimiwa Waziri haoni sasa kuna umuhimu wa kupandisha hadhi hizi zahanati ambazo ziko kwenye kata zinazozunguka kata hii ya Kinesi ikiwemo Kata ya Kyang’ombe, Banaki, Komuge na Kisumwa ili zile zahanati ziweze kutoa huduma kama vituo vya afya kukisaidia hiki kituo cha afya cha Kinesi population wide inayokwenda pale?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili la nyongeza Mheshimiwa Waziri huoni kuna umuhimu sasa kwa muktadha wa majibu haya hiki Kituo cha Kinesi angalau wpaate ambulance ili iweze kuwasaidia kwa umbali huo wa kilometa 40 wanaosafiri hasa tunapopata wagonjwa wa dharura kama akinamama wajawazito na wagonjwa wengine ambao wako serious kwenye matatizo kama haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Wambura Chege kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwatetea wananchi wa Jimbo la Rorya na kuhakikisha wanapata huduma bora za afya ili tuhakikishe kwamba wananchi wale wanaona matunda mazuri ya Serikali yao.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kituo hiki cha afya kinahudumia wananchi wengi katika vijiji takribani 27 na ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali imeendelea kutoa fedha zaidi ya shilingi milioni 900 katika kituo hicho; kwanza, kuhakikisha majengo yanakamilika lakini pia kuendelea kukipanua kituo kile ili kiendelee kutoa huduma bora kwa hao wananchi wengi ambao kituo kinawahudumia. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba tutaendelea kukiboresha kituo kile cha afya, lakini pia zahanati zinazozunguka kituo cha afya, sera na mpango wa maendeleo ya afya msingi tunahitaji kituo cha afya katika kila kata na kila zahanati katika kila Kijiji. Kwa hiyo, kama kuna zahanati ambazo ziko nje ya kata ilipo Kituo cha Afya cha Kinesi tunaweza kupanddisha hadhi zahanati hizo zikawa Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la ambulance, ni kweli tunahitaji kuwa na magari ya wagonjwa kwa ajili ya dharura na tutakwenda kuweka mpango wa kuhakikisha kituo hiki cha Kinesi kinapata gari la wagonjwa ili kiweze kurahisisha huduma za rufaa.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwashukuru sana wananchi wa Kata ya Mtikwa kunipa kura nyingi sana bila shuruti. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kuuliza swali la nyongeza kwa kuwa jumatatu ya pasaka mimi na Naibu Waziri wa Afya tulikwenda kuiona zahanati hii ya Kata ya Mtii na kwa kuwa wananchi wale wamefanya jitihada, niliyeanza kujenga ile zahanati ni mimi na wananchi, sasa wananchi walichomlilia Naibu Waziri wa Afya, wanaomba wajengewe nyumba ya Mganga.

Je, Serikali hamuoni kwamba wananchi wangu wamejitahidi sana kujenga zahanati ile wao wenyewe na Mbunge wao na Mbunge alipokuja aliweka kitu kidogo mkatusaidia kujenga nyumba ya mganga wa zahanati ile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba nimpongeza sana Mheshimiwa Mbunge Anne Kilango Malecela na wananchi wa Jimbo la Same Mashariki kwa kazi kubwa walioifanya kuanzaujenzi wa Zahanati ya Mtii, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge amekuwa karibu sana na wananchi, amefanya ziara pale na Mheshimiwa Naibu Waziri wa Afya na wameona kazi nzuri inayoendelea na wananchi wanatambua mchango mkubwa wa Serikali ambao unaendelea kutolewa katika ujenzi wa zahanati ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kama nilivyojibu kwenye swali la msingi tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya Zahanati ya Mtii, lakini pamoja na kuweka bajeti kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya mganga katika zahanati ile. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Njombe Mjini na sisi tuna Kituo cha Afya ambacho kina uhitaji wa wodi ya kibaba na wazazi na huduma ya upasuaji na Serikali ilishaonesha nia ya kutusaidia.

Swali, je, ni lini sasa shughuli ya ujenzi na ukarabati wa kituo cha afya cha muda mrefu sana Njombe Mjini utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Jimbo la Njombe Mjini kuna Kituo cha Afya cha Mji Mwema na cha siku nyingi ambacho kina uhitaji mkubwa wa miundombinu ya wodi ya akina baba akina mama lakini na wodi ya watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti ya mwaka huu wa fedha tumetenga fedha kwa ajili ya kwenda pia kuongeza miundombinu katika Vituo vya Afya na nimuhakikishie kwamba Kituo cha Afya cha Mji Mwema katika Jimbo la Njombe Mjini nacho kitapewa kipaumbele.
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Ahsante. Pamoja na majibu mazuri ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili nyongeza. Swali la kwanza: Je, ni lini Serikali itaanza kupanga vituo vya afya kutokana na wingi wa watu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Sera ya Serikali ni kila Kata kuwa na Kituo cha Afya na Kila Mtaa uwe na Zahanati: Je, ni lini Serikali italeta vituo vya afya katika Kata ya Kimanga, Kisukuru, Buguruni pamoja na Minazi Mirefu ili hawa wananchi waweze kuondokana na matatizo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Ni kweli kwamba tunajenga Vituo vya Afya, Zahanati na Hospitali za Halmashauri katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuzingatia: kwanza, ukubwa wa kijiografia wa maeneo hayo; na pili, idadi ya wananchi katika maeneo husika ili kuhakikisha vituo vile vinasogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Bonnah kwamba Serikali imeendelea kujenga vituo vya afya kwa kuzingatia vigezo hivyo viwili; kigezo cha ukubwa wa jimbo au halmashauri na pia kigezo cha idadi ya wananchi. Kwa mfano, katika Jiji la Dar es Salaam, miaka miaka mitano iliyopita, zaidi ya vituo vya afya 12 vimeendelea kujengwa na Hospitali za Wilaya zimeendelea kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha ujao wa 2021/2022 katika Manispaa ya Ilala kwa maana ya Jiji la Dar es Salaam peke yake, kuna vituo vya afya vipatavyo sita vitakwenda kujengwa, pamoja na Hospitali ya Halmashauri na katika Halmashauri zote za Jiji la Dar es Salaam zitakwenda kujenga angalau vituo vya afya vitatu. Kwa hiyo, tunaona Serikali imeendelea kuhakikisha inaongeza idadi ya vituo vya afya katika Manispaa na Jiji la Dar es Salaam kwa kuzingatia idadi ya wananchi; na suala hili linafanyika kwa utaratibu huu nchini kote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Sera ya Serikali ya Mpango wa Maendeleo ya Msingi ni kuhakikisha kila Kata inakuwa na Kituo cha Afya na Zahanati katika Vijiji. Sera hii imeendelea kutekelezwa kwa vitendo na Waheshimiwa Wabunge wamekuwa mashahidi kwamba Serikali imewekeza kwa kiasi kikubwa sana katika ujenzi wa zahani na vituo vya afya katika kata zetu. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi kwa vituo vya afya ambavyo tayari Serikali imeanza kujenga na katika kata hizo ambazo Mheshimiwa Kamoli amezitaja. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Jitihada za kujitolea ambazo wananchi wa Jimbo la Segerea wamezionesha, zinafanana sana na jitihada ambazo wananchi wa Jimbo la Nkasi Kaskazini wamezionesha katika kata 17 tunavituo vya afya viwili lakini kuna vituo ambavyo tayari vimeanzishwa kwa nguvu za wananchi. Ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye Kata ya Kabwe ili kuheshimu na kuendelea kuhamasisha wananchi kujitolea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini pamoja na wananchi wa Nkasi Kaskazini kwa kazi kubwa ambayo wameendelea kuifanya kuhakikisha wanachangia nguvu zao katika ujenzi wa miradi ya maendeleo vikiwemo vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua na inathamini sana nguvu za wananchi na tutaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma ambayo wananchi wameanza kuyajenga kwa nguvu zao na mfano mzuri katika bajeti ya mwaka ujao maboma zaidi ya 108 kwa maana ya vituo vya afya vitakwenda kujengwa kwa mapato ya ndani ya halmashauri na vituo vya afya 18 vitakwenda kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna vile zahanati maboma 578 yatakwenda kujengwa.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba katika mpango huu ujao pia katika Jimbo hili la Nkasi Kaskazini tutakwenda kulipa kipaumbele kuhakikisha kwamba wananchi wanaona matunda ya Serikali yao katika kujali nguvu ambazo wameziweka katika maboma yale.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja dogo la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imeendelea kutenga fedha na kupeleka fedha kwenye Hospitali ya Wilaya ya Kivule na tayari Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imepokea shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi na shilingi milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Afya ya Kinywa na Meno.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kutenga fedha na kupeleka kwenye Kituo cha Afya cha Mama na Mtoto, Chanika ili kiweze kujengewa wodi na kuweza kupanda hadhi kuwa hospitali kwa kuzingatia mahitaji makubwa ya wananchi wa Kata za Chanika, Zingiziwa, Msongola, Majohe na Buyuni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Jerry Silaa kwa kusimamia kwa karibu sana miradi mbalimbali ya maendeleo katika Jimbo la Ukonga. Kwa kweli Serikali imeendelea kushirikiana sana kwa karibu na wananchi pamoja na Mbunge wa Ukonga kuhakikisha vituo vya afya hivyo alivyovitaja Kivule na pia kuhakikisha fedha zaidi ya shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu mbalimbali zimepelekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Chanika kwa sasa kinatoa huduma kwa akina mama wajawazito, lakini Serikali inaona kuna kila sababu ya kutenga fedha ili kuongeza miundombinu ya huduma za afya katika Kituo cha Afya cha Chanika ili pamoja na huduma za Afya ya Mama na Mtoto kianze kutoa huduma nyingine kwa wagonjwa ili kusogeza huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba katika mipango ya Serikali, tutakipa kipaumbele Kituo cha Afya cha Chanika ili kiweze kupata fedha kwa ajili ya kujenga miundombinu hiyo na kuhakikisha kwamba huduma zote za afya zinasogezwa kwa wananchi.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Niishukuru Serikali kwa majibu mazuri ambayo Naibu Waziri amewasilisha, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; wananchi wa Kata hii ya Imalamate yenye vijiji vitatu, kwa maana ya Mahwenge, Imalamate pamoja na Jisesa, wamejitolea sana kwa kujenga maboma ya kisasa ya zahanati. Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kuifanya kata hii kuwa moja ya kata za mfano ambazo wananchi wamejitolea kwa kujenga maboma haya ili waipatie kipaumbele cha kukamilisha maboma haya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, Naibu Waziri yuko tayari sasa baada ya Bunge baada ya Bunge hili la Bajeti kuambatana pamoja nami ili kwenda kuwatembelea wananchi wa Kata ya Imalamate kuona kazi kubwa ambayo wameifanya ambayo itakuwa ya kuigwa katika nchi yetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kwa kazi kubwa sana anayoifanya ya kuhakikisha anawasemea wananchi wake na kufuatilia miradi mbalimbali ya maendeleo ikiwemo miradi ya huduma za afya. Pia niwapongeze sana wananchi wa Kata hii ya Imalamate na wananchi wa Busega kwa ujumla kwa kuendelea kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa miundombinu ya kutoa huduma za afya kwa maana ya zahanati na vtuo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua na inathamini kwamba wananchi hawa wameendelea kutoa nguvu zao. Na ni kweli, ni moja ya kata ambazo zimefanya vizuri katika ujenzi wa vituo vya afya na hivyo katika mwaka ujao wa fedha, tumetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya maboma matatu katika Jimbo la Busega. Kwa hiyo bila shaka fedha hizi zitakwenda kukamilisha majengo haya katika Kata ya Imalamate.

Mheshimiwa Naibu Spika, niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge kwenda kushirikiana naye kuwahudumia wananchi wa Busega, lakini pia kutambua michango yao. Hivyo baada ya kikao hiki, tutapanga na Mheshimiwa Simon Songe tuweze kuona lini muda muafaka tutaambatana kwenda Jimboni kwake Busega.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wananchi wa Jimbo la Meatu wapo wanaotembea hadi kilometa 40 kwenda tu kufuata huduma za afya katika zahanati. Je, ni lini Halmashauri ya Wilaya ya Meatu italetewa fedha za kukamilisha maboma katika ule utaratibu wa kukamilisha maboma matatu kwa mwaka 2020/ 2021?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza sana Mheshimiwa Leah Komanya kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwasemea wananchi wa Meatu, lakini pia kuhakikisha miradi ya huduma za afya inakamilishwa na kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Jimbo la Meatu ni jimbo kubwa na wananchi wanafuata huduma za afya mbali kutoka kwenye makazi yao. Ndiyo maana Serikali imeweka mpango wa maendeleo ya afya msingi kuhakikisha tunajenga zahanati katika kila kijiji, vituo vya afya katika kata ili kusogeza huduma hizi kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie kwamba katika mwaka huu wa fedha 2020/2021, Serikali ilitenga shilingi bilioni 27.75 na tayari imekwishatoa shilingi bilioni 23 katika majimbo na wilaya zipatazo 133 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma matatu kwa kila halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimhakikishie kabla ya mwisho wa mwaka huu wa fedha, Juni 30, Jimbo la Meatu pia litakuwa limepata fedha zile shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo. Hili ni sambamba na majimbo na halmashauri zote ambazo bado hazijapata milioni 150, shughuli hiyo inaendelea kutekelezwa na kabla ya Juni 30, fedha hizo zitakuwa zimefikishwa katika majimbo hayo.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tatizo lililoko Busega linafanana kabisa na tatizo lililoko katika Jimbo la Magu. Jimbo la Magu lina vijiji 82, vijiji 40 vina zahanati, vijiji 42 havina zahanati. Tunavyo vijiji 21 ambavyo vimekamilisha maboma ya zahanati. Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia maboma hayo 21 ambayo yanahitaji bilioni moja na milioni 50 ili wananchi waweze kupata huduma kama inavyosema Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwamba kila kijiji kiwe na zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniventura Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali inaendelea kujenga vituo vya afya na zahanati katika vijiji na kazi kubwa imekwishafanyika nchini kote ikiwepo katika Jimbo la Magu. Hata hivyo, ni kweli kwamba bado kazi ni kubwa, bado kuna vijiji vingi na kata nyingi ambazo bado zinahitaji kujenga vituo vya afya na zahanati. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Kiswaga kwamba Serikali itaendelea kutenga fedha kila mwaka wa fedha kuhakikisha tunaendelea kujenga vituo vya afya na zahanati nchini kote, lakini pia katika Jimbo hili la Magu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitambue kwamba katika mwaka huu wa fedha, tayari Jimbo la Magu limeshapelekewa milioni 150 kwa ajili ya kuchangia nguvu za wananchi kujenga na kukamilisha maboma matatu na katika mwaka ujao wa fedha pia imekwishatengewa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati. Kwa hiyo maboma haya yote yaliyobakia pamoja na nguvu za mapato ya ndani ya halmashauri, Serikali itaendelea kutenga fedha kuhakikisha maboma haya yanakamilika na kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa kuwa hali ilivyo katika Jimbo la Busega inafanana kabisa na hali ilivyo katika Jimbo la Sumve. Katika Kata ya Mwabomba wananchi wamejenga maboma katika Vijiji vya Mwambomba, Mulula na Ngogo na mpaka sasa maboma haya hayajamaliziwa, ni maboma ya zahanati. Mheshimiwa Waziri, ni lini sasa Serikali itamalizia maboma haya ili wananchi wa Kata ya Mwabomba na wenyewe wapate huduma ya afya kama yalivyo maeneo mengine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasalali, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata hii ya Mwabomba katika Jimbo hili la Sumve, ni kweli kwamba wananchi wameendelea kuchanga nguvu zao kwa ajili ya ujenzi wa maboma ya zahanati na katika vijiji hivi vitatu, kwanza niwapongeze sana kwa kutoa nguvu zao na kujenga maboma haya kuonesha kwamba kimsingi wana uhitaji mkubwa wa huduma za afya. Ndiyo maana Serikali imeendelea kutambua na kuthamini sana nguvu za wananchi kwa kutenga fedha kwa ajili ya kila jimbo kupelekewa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma haya ya zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo katika Jimbo la Sumve pia, nimhakikishie Mheshimiwa Kasalali kwamba fedha zimetengwa kwa mwaka ujao wa fedha, maboma matatu, ambayo yanahitaji kwenda kukamilishwa yatakwenda kukamilishwa. Nimweleze Mbunge, kwa kuwa vipaumbele ni haya maboma matatu na tayari milioni 150 zimetengwa kwa ajili ya maboma hayo, kwa hiyo tatizo hilo limeshapatiwa majawabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala hili ni endelevu. Katika kila mwaka wa fedha tutaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma yote yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuendelea kuimarisha huduma za afya kwa wananchi wetu.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Changamoto zilizopo kule Busega zinafanana sana na changamoto ambazo tunazo Arumeru Mashariki. Wananchi Kata za Kikatiti, King’ori, Majengo, Gabobo na Kikwe, wanahangaika kila leo kujenga zahanati wenyewe lakini hatujaona Serikali ikija kutusaidia. Je, Serikali ina mpango gani wa kuja kutupa msaada na sisi tuweze kupata huduma za afya kikamilifu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba wananchi wa Arumeru Mashariki wameendelea kuchangia nguvu zao kujenga maboma ya zahanati na vituo vya afya. Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wale wanaungwa mkono kwa juhudi zao ambazo wanazionesha katika kuwekeza katika miundombinu hii ya huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo pamoja na maboma hayo mengine ambayo Mheshimiwa Dkt. Pallangyo ameyasema, nimhakikishie kwamba, kwanza katika mwaka huu wa fedha ambao tunaendelea, 2020/2021, shilingi milioni 150 kwa ajili ya maboma matatu, kuhakikisha kwamba yanakamilishwa, zimetengwa na zitafikishwa kabala ya tarehe 30, Juni, mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka ujao wa fedha, 2021/21, Serikali pia imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya maboma matatu katika Jimbo hili la Arumeru Mashariki. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Pallangyo kwamba tutahakikisha tunaendelea kutenga fedha za kuchangia nguvu za wananchi kukamilisha maboma ya zahanati na vituo vya afya ili tuendelee kusogeza huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, amekuwa mfuatiliaji wa karibu sana kwa ajili ya wananchi wa Arumeru Mashariki, amehakikisha anasimamia miradi mbalimbali ikiwemo miradi hii ya huduma za afya. Na sisi tumhakikishie kwamba tutaendelea kushirikiana kwa karibu sana na wananchi wa Jimbo la Arumeru Mashariki, lakini pia na Mheshimiwa Dkt. Pallangyo kuhakikisha kwamba tunahudumia wananchi wetu kwa karibu zaidi.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa NaibU Spika, Waziri haoni kwamba kwa namna moja au nyingine anasababisha watumishi hawa kufanya kazi katika mazingira magumu na hasa muda ni mrefu maana Halmashauri ile imeanzishwa mwaka 2013 na tayari kuna baadhi ya watumishi wamekwishastaafu. Kwa hiyo naomba commitment ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika jambo hili hawa wananchi wapiga kura wangu wanakwenda kulipwa lini fedha hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bidyanguze, Mbunge wa Kigoma Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kusema katika majibu yangu ya msingi kwamba tunatambua madeni ya watumishi wetu katika Halmashauri ya Uvinza na Serikali imeendelea kuweka mipango kwa maana ya kutenga fedha kwenye bajeti ili kuhakikisha kwamba hayo madeni yatakwenda kulipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, madeni haya yanalipwa kwa kutumia fedha za matumizi mengineyo kwa maana ya OC, lakini pia fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri.

Na hivyo tunaendelea kuwaelekeza Wakurugenzi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na kwa muktadha huu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Uvinza waanze kutenga fedha kwa ajili ya kuwalipa watumishi wale madeni yao kwa awamu ili watumishi wale sasa waweze kufanya kazi kwa kuwa na motisha kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge anasema.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kubwa zaidi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba na Serikali pia inaendelea kufanya uhakiki wa madeni hayo na kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunawalipa wale watumishi stahiki zao za yale madeni.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naipongeza Serikali kwa juhudi hizi za kuboresha huduma za afya katika Jimbo la Singida Kaskazini ikiwemo maendeleo yanayofanyika kwenye hii Hospitali ya Wilaya pamoja na vifaa tiba na upanuzi wa wodi.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Halmashauri ya Wilaya ya Singida inakabiliwa na upungufu mkubwa sana wa watumishi wa Idara ya Afya, hasa wauguzi pamoja na madaktari: Je, Serikali ina mpango au mkakati gani wa kuhakikisha inaleta watumishi wa kada hii katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida ili kuhakikisha huduma za afya zinapatikana ipasavyo?

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali ilijenga Kituo cha Afya cha Mgori pale ambapo hata wewe ulifika siku ile ulipokuja kuniombea kura; lakini hospitali hii hadi sasa haijaanza kufanya kazi pamoja na kwamba kituo hiki kimekamilika kwa asilimia 100 kwa maana ya majengo; hapana vifaa tiba wala gari la kubebea wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, napenda kujua Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inapeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba pamoja na ununuzi wa ambulance kwa ajili ya kubebea wagonjwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani kwa ufuatiliaji wa karibu sana katika miradi ya maendeleo katika Jimbo lake hili la Singida Kaskazini ikiwepo miradi hii ya afya. Kimsingi ni kweli tunafahamu baada ya kazi kubwa sana iliyofanywa na Serikali ya kujenga miundombinu ya huduma za afya kwa maana ya Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali mpya za Halmashauri, automatically tumekuwa na uhitaji mkubwa pia wa watumishi wakiwemo Waganga, Madaktari pamoja na Wauguzi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuweka mipango ya kuendelea kuajiri watumishi hawa ili sasa vituo hivi ambavyo vimejengwa na kukamilika vianze kutoa huduma; na katika mwaka ujao wa fedha, Serikali imeomba vibali vya ajira kwa ajili ya wataalam hawa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ighondo kwamba pamoja na maeneo mengine kote nchini, Serikali itahakikisha inawapangia watumishi katika Halmashauri ya Singida likiwemo Jimbo hili la Singida Kaskazini ili vituo vya afya viendelee kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Mgori kimekamilika muda mrefu na sasa kinahitaji kupata watumishi kama ambavyo nimeongea kwenye swali langu la msingi, pia gari la wagonjwa na vifaa tiba. Katika mwaka ujao wa fedha tumetenga fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba kwa ajili ya Vituo vya Afya na Hospitali za Halmashauri mpya ambazo zinaendelea kukamilishwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakipa kipaumbele sana Kituo cha Afya cha Mgori ili na chenyewe kipate vifaa tiba na kuhakikisha kwamba kinaanza kutoa huduma.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na magari ya wagonjwa, utaratibu wa Serikali tunaendelea kuandaa mipango ya kupata magari ya wagonjwa katika Vituo vya Afya na Hospitali za Halmashauri kwa awamu kwa kadri ambavyo tutapata fedha. Hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hicho pia ni kipaumbele na Serikali itakwenda kukitimiza.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa ajili ya majibu mazuri ya Serikali, lakini naamini Naibu Waziri yeye mwenyewe ameona namna ambavyo changamoto ni kubwa. Hii ni Hospitali ya Wilaya yenye takriban wakazi 200,000 na kwa mwaka mzima wa fedha tumepewa shilingi milioni 53. Kwa hiyo, anaweza akaona ukubwa wa tatizo ulivyo na kwamba haiwezi kututosheleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo basi, swali langu la nyongeza sasa: Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kutujengea vituo vingine vya Afya katika Jimbo la Iringa Mjini, hasa katika Kata za Kitwilu, Igumbilo, Nduli, Isakalilo na Mkwawa ili angalau kupunguza mzigo katika Hospitali ya Frelimo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, ni lini Serikali itaufanyia kazi mpango au ombi letu tulilolileta kama mkoa la kuomba sasa hospitali hizi zibadilishane maeneo; pale ilipo hospitali ya wilaya ijengwe ya mkoa na ile ya mkoa tuachiwe wilaya kutokana na eneo finyu lililopo katika hospitali yetu ya wilaya ili kufanya utanuzi zaidi kwenye eneo la hospitali ya mkoa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jesca Jonathan Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali hii ya Frelimo ni hospitali ya Manispaa ya Iringa na kama ambavyo nimeeleza kwenye jibu langu la msingi, hospitali hii bado ina upungufu mkubwa wa miundombinu kwa maana ya wodi kwa ajili ya kulaza wagonjwa; wodi ya wanaume, wodi ya watoto lakini pia wodi ya akinamama. Hii imepelekea pamoja na umuhimu wa hospitali hii kuhudumia wagonjwa wachache zaidi ikilinganishwa na hadhi ya hospitali yenyewe. Nndiyo maana kwa vigezo vile vya mgao wa fedha za ruzuku, inapata fedha kiasi hicho ambacho kimsingi lengo la Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatenga fedha kwa ajili ya kuongeza wodi katika hospitali ile ili ihudumie wananchi wengi zaidi na mgao wa fedha uweze kuongezeka Zaidi. Katika mwaka ujao wa fedha tumetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunajenga wodi hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na ombi la kujenga vituo vya afya katika kata hizi za Kitwiru, Igumbiru, Mkwawa na nyingine nilizozitaja, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi ni kujenga vituo vya afya katika kila kata na nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge amekuwa mstari wa mbele sana kuhamasisha wananchi kujitolea nguvu zao kuanza ujenzi wa vituo hivi na sisi kama Serikali tutaendelea kumuunga mkono kuhakikisha tunatenga fedha katika bajeti zijazo kuunga mkono nguvu za wananchi katika kujenga vituo vya afya katika kata hizi kwa awamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni kweli kwamba Mkoa wa Iringa umewasilisha mapendekezo kwa kufuata taratibu zote kuomba Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa iweze kubadilishana na hospitali ya rufaa ya mkoa. Sisi kama Serikali tumepokea mapendekezo hayo kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutayafanyia kazi na tathmini maombi hayo. Baada ya hapo tutatoa maamuzi ya Serikali ili kuhakikisha kwamba tunaboresha miundombinu ya huduma za afya katika Mkoa wa Iringa.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu haya ya Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna haja ya kukaa nae baadaye tuangalie hizi takwimu vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na majibu hayo ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza. Swali la kwanza, moja ya sababu kubwa ya upungufu wa watumishi kwenye Halmashauri za Vijijini kama ilivyo Halmashauri ya Korogwe au kama ilivyo kwenye Jimbo la Mlalo kule kwa ndugu yangu Shangazi, sababu kubwa ni kwamba watumishi wanaenda kule, wakipata ajira wanahama. TAMISEMI mmekuwa mkipitisha uhamisho wa watumishi wakati mwingine bila kuzingatia maoni ya wakurugenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kujua ni lini sasa TAMISEMI mtakubali kuzingatia maoni ya Wakurugenzi kutoa watumishi mbadala kabla ya kuwahamisha waliopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; wakati mwingine tunaweza kupunguza shida ya upungufu wa walimu kwa kusawazisha Ikama ndani ya halmashauri yenyewe. Kwa mfano Halmashauri ya Korogwe zaidi ya miaka mitatu kifungu cha moving allowance hakijawahi kupat afedha. Inasababisha ugumu katika kusawazisha Ikama ya watumishi ndani ya halmashauri yetu. Ni lini Serikali itakuwa tayari sasa kutoa fedha ya kutosha kwenye vifungu hivi vya uhamisho ili kuweza kusababisha Ikama ndani ya Halmashauri yenyewe? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na changamoto ya upungufu wa watumishi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa ikiwemo Halmashauri ya Korogwe. Lakini kama ambavyo nimetangulia kutoa m ajibu ya msingi kwamba Serikali imeendelea kuweka jitihada za kutosha kuhakikisha kwamba tunaendelea kuongeza watumishi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni kweli tumekuwa na changamoto kubwa sana ya watumishi hasa wanaokuwa katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa maeneo ya vijijini kuomba uhamisho wengi wao wakiomba kuhamia mijini. Ofisi ya Rais TAMISEMI na Serikali kwa ujumla imeendelea kuhakikisha inazingatia Ikama katika maeneo ya vijijini na imeendelea kuhakikisha inasimamia kwa karibu uhamisho wa watumishi hasa kutoka vijijini kwenda mijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba si kweli kwamba TAMISEMI imekuwa kila siku inapitisha maombi ya uhamisho kwa watumishi wote wanaoomba. Mara kwa mara tumekuwa tunachuja sababu za msingi ambazo zinasababisha baadhi ya watumishi kukubali lakini watumishi walio wengi kutokukubaliwa kupata uhamisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili Serikali imeweka utaratibu sasa. Ofisi ya Rais TAMISEMI tutaenda kuzindua mfumo wa kielektroniki ambao sasa maombi ya uhamisho yatapitishwa kwa njia ya kielektroniki na yatawezesha sasa kuchuja kwa uhakika zaidi hamisho zote ambazo zinaombwa na itawezesha sana watumishi wetu katika maeneo ya vijijini kubakia kufanya kazi katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili tutakwenda kuwa na mikataba ya watumishi wanaoajiriwa. Watumishi wengi wamekuwa wakiajiriwa maeneo ya vijijini, wakifika na kupata cheque number wanaanza kufanya jitihada za kuhama. Sasa kabla ya kuajiriwa tutahakikisha tunakuwa na mikataba kwamba baada ya kupangiwa kwenye vituo hivyo ni lazima wakae angalau miaka mitatu au mitano kabla ya kuanza kuomba vibali vya uhamisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii itatuwezesha sana kuhakikisha watumishi wetu katika maeneo ya vijijini wanabaki na kutoa huduma ambazo zinakusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ugumu wa kusawazisha watumishi kwa maana ya ikama katika maeneo yetu, ni kweli na Serikali imeendelea kutenga fedha za matumizi mengineyo kwa awamu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha kuhakikisha yale maeneo ambayo yana watumishi wengi lakini maeneo mengine yana watumishi wachache tuweze kufanya usambazaji wa ndani ya halmashauri. Hili pia tumeendelea kusisitiza Wakurugenzi katika Serikali za Mitaa kutenga bajeti za uhamisho wa ndani katika halmashauri zao ili waweze kuhakikisha mgawanyo wa watumishi ndani ya halmashauri unazingatia ikama na angalau unakuwa reasonable.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tutaendelea kutenga fedha kuhakikisha msambao huu pia unakuwa wenye tija zaidi. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa changamoto ya upungufu wa watumishi iliyoko Wilaya ya Korogwe ni sawa sawa kabisa na iliyoko Jimbo la Babati Vijijini hasa Sekta za Afya na Elimu. Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza tatizo hili la watumishi hawa? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tuna upungufu wa watumishi lakini kama ambavyo nimetangulia kusema kwenye jibu la msingi, Serikali imeendelea kutenga ikama kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaendelea kuandaa na kuomba vibali vya ajira kila Mwaka wa Fedha ili kuendelea kuongeza idadi ya watumishi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Kwa hivyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Baran kwamba katika Wilaya ya Babati pia tutahakikisha tunaipa kipaumbele katika ajira za Mwaka wa Fedha ujao ili angalau tuendelee kuboresha idadi ya watumishi katika halmashauri hiyo.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi. Wilaya ya Misenyi ni Wilaya yenye Kata 20. Inavyo vituo vya afya viwili ambavyo havina watumishi kabisa pamoja na Idara za Elimu na Kilimo. Je, ni lini Serikali itaweza kutupatia watumishi wa kutosha ili watoe huduma nzuri kwa wananchi wa Wilaya ya Misenyi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha ujao 2021/2022 Serikali na Ofisi ya Rais – TAMISEMI tumeomba vibali vya ajira takribani 12,000 kwa ajili ya watumishi wa kada mbalimbali katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa na hivyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Kyombo kwamba katika mgawanyo wa watumishi katika Mwaka ujao wa fedha tutahakikisha tunaitazama Halmashauri ya Misenyi kwa jicho la karibu ili tuendelee kuboresha huduma za afya katika vituo hivi ambavyo havina watumishi lakini pia katika kada nyingine katika halmashauri hiyo na kote nchini kwa ujumla wake.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba niulize hivi, Je, Wizara ya TAMISEMI haioni umuhimu wa kuweka maafisa masoko kwenye halmashauri zetu. Tunajua kwamba tatizo kubwa kwenye halmashauri ni ukosefu wa masoko. Watu hawajaunganishwa na masoko, sasa tungekuwa na maafisa hawa wangetusaidia sana. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, katika uendeshaji wa shughuli za masoko katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Serikali imeweka utaratibu ambao pamoja na wakuu wa idara wengine, wakuu wa idara ya fedha na biashara kuna maafisa biashara katika halmashauri zetu ambao kimsingi wanafanya kazi kwa karibu ambazo zinafanana sana na Maafisa Masoko.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo tunaendelea kuhakikisha kwamba tunaboresha mfumo huo kuhakikisha kwamba wale maafisa biashara ambao wanasimamia masoko na shughuli nyingine zote za biashara katika halmashauri wanafanya kazi zao kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wazo lake pia la kuwa na Maafisa Masoko tunalichukua, tutalifanyia tathmini na kuona kama tunaweza tukaongeza nguvu katika eneo hilo kuwa na maafisa biashara na pia kuwa na maafisa masoko. Kwasababu lengo la Serikali ni kuhakikisha kuna ufanisi mkubwa wa biashara na ustawi wa mapato ya ndani lakini pia ya wananchi katika masoko yetu.
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina swali la nyongeza. Wakati mwingine wananchi wetu wanakwenda kwenye vituo vya kutolea huduma za afya wanakosa dawa siyo kwa sababu dawa hiyo inakuwa haipo kwenye maghala ya MSD, bali ni matatizo ya uagizaji ambayo yanatokana na vituo vyetu vya kutolea huduma za afya kutokuwa na hawa watu muhimu wafamasia na wateknolojia dawa ambao wana utaalam wa kuratibu, ku-forecast na kujua kwamba kipindi hiki tuagize dawa gani, kipindi hiki kuna mlipuko wa magonjwa fulani, kuwe na dawa fulani. Sasa ili kuhakikisha kwamba watu hawa muhimu wanakuwepo muda wote katika vituo vya kutolea huduma za afya:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuruhusu Ma-DMO na Wakurugenzi wa Halmashauri zenye uwezo ku-engage watu hawa ili wawepo muda wote hata kwa mtindo wa internship au mikataba ya muda wakati tukisubiri hizi ajira?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kimsingi tunafahamu kwamba katika vituo vyetu vya huduma za afya kama ambavyo nimetangulia kueleza kwenye jibu la msingi, tuna upungufu wa wataalam hawa wa teknolojia wa dawa na wateknolojia wasaidizi wa dawa. Ni kweli kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge Zedi ameelezea, tunahitaji kuwa na wataalam hawa ili kuhakikisha vituo vyetu vinaweza kuweka maoteo mazuri ya dawa lakini pia uagizaji kulingana na utaalam ili kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, pamoja na jitihada hizi za Serikali, pia Serikali ilishatoa maelekezo kwa Wakurugenzi, kwa Halmashauri zile ambazo zina uwezo wa mapato ya ndani ya kuwaajiri kwa mikataba wataalam hawa, waweze kuwaajiri na kuwasimamia kwa karibu chini ya DMO kuhakikisha huduma hizi za upatikanaji wa dawa katika vituo hivyo zinaboreshwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba jambo hilo lishafanyiwa kazi na Serikali na nitoe wito kwa Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kutumia fursa hiyo kwa wale ambao wana uwezo wa kuwaajiri ili tuboreshe huduma za afya kwa wananchi.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka tumekuwa tunaongeza bajeti ya dawa katika Serikali yetu na tumekuwa tukiona bado zahanati na vituo vya afya havipati dawa. Swali langu: Je, mmefanya utafiti gani wa kuhakikisha kwamba hizo fedha, shilingi bilioni 270 na hiyo shilingi bilioni 140 ndizo zitakwenda kutatua changamoto ya dawa katika zahanati zetu na vituo vya afya?

Swali langu la pili; hivi tunavyozungumza wananchi wenye changamoto hizi wa kutoka Jimbo la Kalenga na wengine wengi wanaangalia; je, wananchi wategemee nini kuwa hizi dawa katika zahanati na vituo vya afya itakuwa ni historia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama ambavyo Mheshimiwa Grace Victor Tendega ametangulia kusema, Serikali imeendelea kuongeza bajeti ya fedha kwa ajili ya ununuzi wa dawa, vitendanishi na vifaa tiba kwa takriban mara tisa ndani ya miaka mitano na hii ni kwa sababu Serikali inajali sana wananchi na inahitaji kuona wananchi wanapata dawa za kutosha ili kuhakikisha kwamba huduma za afya ni bora zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo ni kweli kwamba bado tuna changamoto ya uhitaji wa dawa na Serikali inatambua kwamba bado tuna kazi ya kufanya kuhakikisha tunaendelea kupunguza sana upungufu wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu vya huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana katika jibu langu la msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali imepeleka fedha mpaka sasa, zaidi ya shilingi bilioni 140 zimepelekwa katika vituo vyetu na mpaka mwisho wa mwaka huu wa fedha, ifikapo Juni, tutakuwa tumepeleka fedha zaidi kuhakikisha tunaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa katika vituo hivyo na kwa makundi maalum na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimhakikishie kwamba Serikali imefanya tathmini kwamba kadri inavyoongeza fedha ndivyo upungufu wa dawa unavyopungua na ndiyo maana lengo la Serikali ni kuendelea kuongeza fedha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kuboresha upatikanaji wa dawa na kuondoa kabisa upungufu wa dawa katika vituo vyetu.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru sana. Kusema kweli Serikali imetenga fedha nyingi. Kwenye Jimbo letu la Vunjo Kata 16 hakuna kituo cha afya cha Serikali isipokuwa vituo vikongwe, vichakavu vya Mwika, OPD Himo na Kiruavunjo. Ni chakavu hata havistahili kuitwa vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri atueleze ni lini watakarabati vituo hivi na kuviinua hadhi ili viweze kuwa vituo vya afya vinavyotumika na watu wa Vunjo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi tunatambua sana kwamba katika Jimbo la Vunjo kuna upungufu mkubwa wa vituo vya afya lakini hata vile vituo vya afya ambavyo vipo, vina uchakavu kwa sababu ni vya siku nyingi. Ndiyo maana katika mpango wetu ambao tumeuwasilisha na bajeti yetu ya mwaka 2021/2022 tumeweka kipaumbele kwanza cha kwenda kuhakikisha tunajenga vituo vya afya 211 katika maeneo ambayo hayana vituo vya afya.

Pili, kuhakikisha tunaweka mpango wa kwenda kukarabati na kupandisha hadhi vile vituo ambavyo vina sifa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba Jimbo la Vunjo pia litapewa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunafanyia kazi vituo hivyo vya afya. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru sana kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini niseme kwamba Hospitali ya Frelimo ilijengwa ili kupunguza msongamano mkubwa sana uliopo katika Hospitali yetu ya Mkoa na mpaka sasa hivi tunashukuru kwamba tumeweza kupata milioni 500, lakini hakuna hata wodi moja toka mwaka 2012 imeanzishwa, lakini pia tushukuru kwa hizi shilingi milioni 400 ambazo tumepewa kwa ajili ya kujenga majengo ya maabara na uchunguzi.

Sasa ni lini Serikali italeta vifaa kama vya X-Ray, MRA, CT Scan ili sasa wananchi wa Iringa wasiendelee kwenda kwenye Hospitali ya Mkoa?

Mheshimiwa Naibu Spika, Swali langu la pili, Sera ya Serikali ni kujenga vituo vya afya kila kata. Lakini Manispaa yetu ya Iringa ina kata 18 na ina vituo viwili tu vya Ngome na Ipogolo, vituo ambayo kwa kweli ni vichakavu mno na havijawahi kufanyiwa ukarabati wowote toka vimeanzishwa. Na tulitegemea kwamba hivi vituo…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Ritta Kabati uliza swali.

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Kuna population karibu ya watu laki mbili.

Je, ni lini Serikali sasa hivi itaboresha hivi vituo vya afya ili viweze kufanya huduma ya upasuaji ili kupunguza msongamano mkubwa uliopo katika Hospitali yetu ya Mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza namshukuru kwa kutambua kwamba Serikali imeendelea kuwekeza fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Hospitali hii ya Manispaa ya Iringa - Frelimo inatoa huduma na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimhakikishie kwamba, kama ambavyo tumeweka katika mipango yetu katika mwaka wa fedha ujao tutaendelea kutenga fedha kwa awamu ili kuhakikisha wodi zote katika hospitali ile zinajengwa, zinanakamilika ili ziweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi wa Manispaa ya Iringa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nimhakikishie kwamba vifaa tiba ni moja ya kipaumbele cha Serikali na ndio maana katika bajeti yetu 2021/2022 tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 14 kwa ajili ya kununua vifaa tiba katika vituo vyetu na hospitali zetu. Kwa hiyo, nimuhakikishie hospitali hii pia itapewa kipaumbele kuhakikisha kwamba tunakwenda kupeleka vifaa tiba katika hospitali ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tatu kuhusiana na vituo vya afya tutaendelea kujenga na katika mwaka wa fedha ujao Manispaa ya Iringa ni moja ya Manispaa ambazo zitajengewa vituo vya afya.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, hali inayoonekana Manispaa ya Iringa yaani inafanana moja kwa moja na hali iliyopo kwenye Halmashauri ya Masasi. Kwa sababu ni kata 18 kama ilivyo, lakini hali kadhalika vituo vya afya viwili na hali ni mbaya kabisa.

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Mchungahela.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu je, ni lini Serikali itatuwezesha kuwa na vituo vya afya zaidi, maana yake vituo viwili vya afya ni vichache?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela, Mbunge wa Jimbo la Lulindi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri ya Masasi Vijijini katika mwaka wa fedha kuna fedha ambazo zimetengwa katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya kujenga vituo vya afya. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie kambwa pamoja na bajeti yetu 2021/2022 kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya afya kwa mapato ya ndani lakini pia kwa fedha za Serikali Kuu tutaendelea kutenga fedha kuhakikisha jimbo hilo pia linapata vituo vya afya.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza.

Kama ulivyosimamia hospitali ya Makandana na kupata wodi ya wanawake bado tunashida ya x-ray wananchi wanaambiwa waende hospitali ya Igogwe. Ni lini Serikali itatupatia x-ray mpya katika hospitali ya Makandana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hospitali ya Halmashauri ya Rungwe maarufu kama Makandana ina tatizo la x-ray pamoja na juhudi za Serikali za kuboresha miundombinu mingine, kipaumbele pia ni kupeleka vifaa tiba zikiwemo x-ray. Na katika mipango ya fedha ya miaka ijayo tutahakikisha pia hasa mwaka ujao katika mgao wa x-ray lakini na vifaa tiba vingine tunaipa kipaumbele Halmashauri ya Rungwe kwa maana ya Hospitali ya Makandana.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Mji wa Tarime mpaka leo imesajiliwa kama Hospitali ya Wilaya na kiuhalisia inahudumia wananchi wote wa kutoka Tarime Vijijini kwa huduma za upasuaji, kutoka Rorya, lakini pia watu wengine wanatoka nje ya nchi kwa maana ya kule Kenya tuko mpakani.

Ningetaka kujua ni kwa nini Serikali haijaifanya hospitali hii ili iweze kupata stahiki kama Hospitali ya Wilaya kama vile ilivyo Hospitali ya Kahama Mjini ambayo inahudumia Ushetu na Msalala, kama vile ilivyo Hospitali ya Nzega Mjini ambayo inahudumia Bukene na Nzega Vijijini ili sasa ihudumie sio kwa idadi ya watu wa Tarime Mji bali kwa idadi ya watu halisia wa kutoka Wilaya nzima ya Tarime na wengine kutoka Rorya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kupelekea kupokea watu wengi nje ya Tarime Mji, hospitali ile inaelemewa, haina matabibu wa kutosha, na kama nilivyosema awali wanaleta fedha chache, leo hata ukienda mortuary unakuta ina burst kwa sababu inachukua watu wote kutoka nje.

Ningetaka kujua ni lini Serikali itapanua chumba cha kuhifadhi maiti ili sasa wakati mkibadilisha usajili kuwa wa Wilaya na kuweka stahiki za Wilaya ili mortuary ile iweze kupokea Watanzania ambao wamekutwa wamefariki na kuja kuhifadhiwa pale Tarime Mji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hospitali ya Mji wa Tarime inahudumia pamoja na wananchi wa kutoka katika Halmashauri za jirani na Tarime na ni utaratibu wa kawaida katika hospitali zetu ambazo mara nyingi zipo mipakani, lakini hata zile ambazo zinahudumia wananchi ambao wapo karibu na Halmashauri hiyo.

Kwa hiyo, kuna baadhi ya hospitali za Halmashauri nchini kote ambazo pamoja na wananchi wa ndani wa Halmashauri husika pia zinahudumia wananchi wanaotoka katika Halmashauri nyingine, ni suala la kawaida na utaratibu wetu sisi katika afya hatuna mipaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nitambue kwamba ni kweli tunafahamu hospitali hii inazidiwa na wagonjwa, lakini takwimu zimeonesha kwa wastani kwa siku wagonjwa wanaolazwa ni 70 lakini pia 140 wa OPD. Na Serikali inatambua kwamba tunahitaji kuendelea kuboresha miundombinu katika hospitali hii na sisi tutaendelea kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi ya watumishi kwa maana ya waganga na wauguzi ili waweze kuendana na mzigo wa hospitali hii. Lakini pia ujenzi wa mortuary ni kipaumbele katika Serikali yetu, lakini pia katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba hili nilichukue ili twende na sisi tukalifanyie tathmini kuona kwa maana Serikali Kuu na Halmashauri namna gani tutafanya ili tuweze kuondoa adha ya kuwa na mortuary ndogo na kuboresha huduma hizi kwa wananchi. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotokea Tarime hata Maswa kinatokea hicho kwamba Hospitali ya Maswa inazidiwa kwa wagonjwa na imekadiriwa kwanza kuwa Hospitali ya Wilaya, lakini inahudumia zaidi ya Wilaya moja. Kuna wagonjwa wanatoka Itilima, wagonjwa wanatoka Wilaya ya Meatu na wagonjwa wa Wilaya ya Maswa. Hospitali inaonekana kama ya Wilaya lakini inazidiwa kwa sababu watu wengi wanakwenda pale.

Kwa hiyo nilikuwa naomba aji-commit Mheshiwa Naibu Waziri je, na Maswa atai-consider na yenyewe iweze kuongezewa hadhi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mbunge wa Maswa Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameongea kuhusiana na Hospitali ya Halmashauri ya Maswa ni hospitali ambayo ni kongwe, lakini ina hudumia wananchi wengi wa ndani ya Halmashauri ya Maswa, lakini pia na Halmashauri zingine kama Itilima na Meatu. Lakini naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali iliona hilo na imelifanyia kazi. Kwanza kwa kujenga Hospitali ya Halmashauri katika Halmashauri ya Wilaya ya Itilima ili kuhakikisha wananchi wa Itilima ambao walikuwa wanalazimika kufika Maswa sasa watatibiwa Itilima, lakni pia imeboresha sana hospitali ya Halmshauri ya Meatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na hayo bado tunatambua kwamba kuna kazi ya kufanya katika Hospitali ya Halmashauri ya Maswa na ni muhakikishie tunaji-commit kwamba tutaendelea kuhakikisha tunaboresha miundombinu, vifaa tiba na upatikanaji wa wataalam ili tuhakikishe hospitali ile inatoa huduma bora zaidi. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Wilaya ya Urambo ina hospitali ya wilaya iliyojengwa mwaka 1975 na hali yake siyo nzuri. Je, Serikali yetu inayosikiliza maombi ya wananchi ni lini itakuja kuingalia itengenezwe upya ili iende na wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Margaret Simwanza Sitta, Mbunge wa Urambo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Urambo ni kweli ni hospitali kongwe sana ambayo imejengwa mwaka 1975 na bahati njema katika ziara yangu pia nilifika katika hospitali ile tukashirikiana vizuri sana na Mheshimiwa Mama Margaret Sitta, tukaikagua hospitali ile na kuona kwa kweli tunahitaji kuweka mpango mkakati wa kuzikarabati hospitali kongwe zote nchini ikiwepo ya Hospitali hii ya Urambo.

Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie kwamba mipango ya Serikali tumeshapanga katika mwaka ujao wa fedha kuanza kukamilisha ujenzi wa Hopitali za Halmashauri katika Halmashauri zote ambazo hazina Hospitali za Halmashauri. Lakini baada ya hapo tutakwenda kwenye awamu ya kukarabati au kujenga kulingana na tathmini hospitali nyingine za Halmashauri katika Halmashauri zenye hospitali kongwe sana ikiwepo Urambo.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba suala hili tunalifanyia kazi na tutahakikisha kwamba tunalitekeleza. (Makofi)
MHE. VITA RASHID KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Kwa kuwa Serikali ilitufanyia kazi nzuri sana Jimbo la Namtumbo kutujengea Kituo cha Afya cha Mtakanini na kukarabati Kituo cha Afya cha Mji wa Namtumbo lakini vituo vya afya hivi viwili havina watumishi.

Je, Serikali ipo tayari sasa kutupangia watumishi ili ifanye kazi kama ilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi ofisi ya Rais - TAMISEMi, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipokee shukrani nyingi za Mheshimiwa Mbunge wa Namtumbo kwa kazi kubwa sana ambayo Serikali imefanya kuhakikisha inakarabati na kujenga vituo vya afya katika Jimbo la Namtumbo. Lakini nimhakikishie kwamba Serikali inatambua sana kwamba tuna upungufu wa watumishi katika vituo vile vya afya. Lakini kama tunavyoona, hivi sasa Serikali imetangaza ajira 2,796 za wataalam wa afya, lakini pia katika mwaka wa fedha tutakwenda kuomba vibali kuhakikisha kwamba tuna ajiri watumishi hawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba Jimbo la Namtumbo litapewa kiupaumbele kuhakikiha tunaendelea kupelekea watumishi pale na kuboresha huduma za afya. (Makofi)
MHE. NICHOLAS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Sasa naomba kuuliza swali la nyongeza kwa Serikali, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Sera ya Afya ya Mwaka 2007, Sura ya 7 imeweka vigezo kwa Hospitali za Kata na Wilaya na moja ya kigezo ni lazima kuwe na gari la wagonjwa. Sasa Serikali imechukua gari la Kituo cha Afya cha Choma imepeleka Igunga na Kituo cha Afya cha Choma tena kimekosa gari. Je, Serikali haioni tunaendelea kukanyanga Sera ambayo tumejitungia sisi wenyewe? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nicholas Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, gari la Kituo cha Afya cha Choma limepelekwa katika Hospitali ya Halmashauri ili kuweza kuboresha zaidi huduma za Halmashauri kwa kuwa Hospitali ya Halmashauri ina wagonjwa wengi zaidi kuliko Kituo cha Afya. Hata hivyo, gari hilo linafanya kazi katika vituo vyote viwili kwa maana Kituo cha Afya na Hospitali ya Halmashauri.
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza niipongeze Serikali na kuishukuru pia kwa kuweza kutupatia fedha hizi ambazo nina uhakika zinakwenda kumaliza Kituo cha Afya cha Uyowa, lakini niendelee kuiomba Serikali basi hiki Kituo cha Mwangozo na chenyewe kiweze kufikiriwa ili kiweze kuendelea kutoa huduma. Hata hivyo, nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa taaluma mimi ni Mwalimu na tunajua vigezo ambavyo vinatumika kuanzisha hizi shule zetu, lakini ningeomba kujua, je, wataalam wa Afya na TAMISEMI huwa wanatumia vigezo gani wanapoamua kujenga hizi zahanati zetu, kwani tunaona baadhi tu ya majengo ndiyo yanajengwa pasipokuwa na maabara ambapo tunajua maabara ndiyo kigezo kimojawapo ili Daktari aweze kutoa huduma vizuri. Je, kwa nini zahanati nyingi huko vijijini hazina maabara?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kama vigezo hivyo vinazingatiwa, je, Serikali sasa haioni umuhimu wa kutujengea hizi maabara katika zahanati zetu ili kuweza kuwapunguzia mzigo hawa wananchi wetu ambao wanatembea umbali mrefu kwenda kufuata huduma za maabara? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Ulyankulu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, napokea pongezi zake kwa Serikali kwa kupeleka fedha shilingi milioni 600 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Uyowa. Pili, vigezo ambavyo vinatumika kujenga zahanati zetu ni michoro ambayo imepitiwa kitaalam na ambayo kimsingi kwa ramani zetu kwa sasa za Ofisi ya Rais, TAMISEMI za zahanati zina provision ya maabara. Kwa hiyo, ramani zote za vituo vya afya, zahanati na Hospitali za Halmashauri zina maabara. Hivyo, tutaendelea kuhakikisha tunatenga fedha kwa awamu kukamilisha yale majengo ya zahanati lakini pia na vyumba vya maabara kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, tunaona of course umuhimu wa kuhakikisha kwamba tunaendelea kujenga maabara na ndiyo maana kwenye swali la msingi nimeeleza ambavyo Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kujenga vituo hivyo zikiwemo maabara katika maeneo hayo.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa niaba ya wananchi wa Mbozi napenda kuuliza swali langu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Hayati Rais Magufuli akiwa kwenye kampeni aliahidi wananchi wa Mji Mdogo wa Mlowo kwamba kutajengwa kituo cha afya kikubwa cha kisasa pale. Tayari wananchi wameshapeleka site matofali 150,000 na tayari heka 10 zimeshatengwa. Sasa ni lini Serikali itapeleka fedha kuanza ujenzi wa kituo hicho cha afya katika Mji Mdogo wa Mlowo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ahadi za Viongozi wetu wa Kitaifa ni ahadi ambazo lazima Serikali tutakwenda kuzitekeleza na hivyo tumeandaa mpango kabambe wa kuhakikisha kwamba tunaratibu utekelezaji wa ahadi zote zilizotolewa na Viongozi wetu wa Kitaifa ikiwemo Kituo cha Afya cha Mlowo katika Jimbo la Mbozi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuweka mpango na kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Mlowo, Mbozi.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali katika Jimbo la Busega imeanzisha vituo vya afya viwili ambavyo mpaka sasa vimeshaanza lakini bado vinakosa wodi ya wazazi, wanaume pamoja na wodi ya wanawake. Nini kauli ya Serikali ili kupeleka fedha kwa ajili ya kumalizia vituo hivyo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imejenga vituo vya afya viwili katika Jimbo la Busega na ujenzi ule unaendelea kwa awamu. Tumejenga awamu ya kwanza lakini tunafahamu kwamba kunakosekana wodi ya wazazi, lakini pia wodi ya wanaume na baadhi ya miundombinu mingine ambayo bajeti ijayo tutatenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakamilisha ujenzi wa miundombinu hiyo.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Wizara; na kwa kuwa katika kundi la vijana wanakopeshwa vijana wa kiume na wa kike; na kutokana na Katiba yetu tunawatambua kwa umri wa miaka 18 mpaka 35; na kwa kuwa kuna wanaume wengi ambao ndiyo bread winner kwenye familia zao na ni wazalishaji kati ya miaka 36 – 45; na kwa sababu ni suala la kisera: Je, Serikali ipo tayari kuongeza umri angalau mpaka miaka 45 katika kundi hili la vijana ili wanaume waweze kufaidika na mikopo hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA – (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali imeweka utaratibu huu wa mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Na katika kundi la vijana asilimia kubwa wanaonufaika na mikopo hii ni vijana wa kiume, lakini definition kwa maana ya tafsiri ya vijana kwa mujibu wa taratibu zetu ni wale wenye umri wa miaka 18 hadi 35. Kwa hivyo, kwa maana ya tafsiri hii ya kisheria Serikali bado haijaweka mpango wa kuongeza umri kwa sababu, lengo la mikopo hii ni kwa vijana na kwa maana ya tafsiri ya vijana ni chini ya miaka 35. Kwa hivyo tunachukua wazo lake, lakini kwa sasa sheria hii itaendelea kutekelezwa wakati tunafanya tathmini ya kuona uwezekano wa kuongeza eneo hilo.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni kweli kwamba, katika halmashauri zetu kunatengwa fedha asilimia 10 kwa maana ya mbili, nne na nne kwa wanawake, lakini ufuatiliaji wa mkopo huu baada ya kupewa hivyo vikundi unakuwa ni mgumu sana kurudisha fedha kwenye halmashauri. Serikali ina mkakati gani wa kudai madeni hayo ili fedha zirudi zikopeshe wanawake wengine kwa wakati unaofuata? Ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa, swali linahusu wanaume nao watapataje access ya hizo fedha?

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, wanaume tunaomba wapate, lakini wanapokwenda kukopa huwa hawaelezi wake zao kama wamekwishakopa mkopo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA – (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mpango huu wa kukopesha asilimia kumi kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu Serikali imeboresha utaratibu kupitia Sheria Na. 12 ya Mikopo kwa maana ya fedha za Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kuhakikisha sasa siku za nyuma hatukuwa na asilimia kwa ajili ya ufuatiliaji wa marejesho ya mikopo hii. Kwa hivyo, ilikuwa ni ngumu kwa Maafisa Maendeleo ya Jamii kufuatilia vikundi ambavyo vimekopeshwa kwa ajili ya kurejesha mikopo ile ili vikundi vingine vinufaike zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini kuanzia mwaka wa fedha ujao tumeweka kifungu cha ufuatiliaji katika vikundi hivyo kuwawezesha Mamlaka ya Serikali za Mitaa na Maafisa Maendeleo ya Jamii kufuatilia vikundi vile pamoja na kuviwezesha kuhakikisha marejesho yanafanyika ipasavyo.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, ni lini sasa tathmini ya uchakavu wa miundombinu ya Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni itaenda kukamilika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa hii hospitali ilianza mwaka 1973 na mwaka 1992 ilipandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Wilaya na kwa kuwa bado inaendelea kutoa huduma katika Wilaya ya Manyoni na kwa kuwa tuna upuungufu mkubwa sana wa wataalam katika hospitali na Jimbo zima la Manyoni Mashariki, nini commitment ya Serikali ya kupeleka wataalam katika Jimbo la Manyoni Mashariki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Manyoni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishaweka utaratibu wa kufanya tathmini katika hospitali zetu zote kongwe na chakavu 43 ambazo tumekwishazitambua ikiwemo hospitali hii ya Manyoni na kazi hiyo tayari imeanza na inaendelea. Tunatarajia ifikapo mwezi wa tatu mwaka ujao tutakuwa tumekamilisha na kufanya maamuzi wapi tutajenga hospitali mpya na wapi tutakwenda kuzikarabati zile hospitali ambazo bado zinahitaji ukarabati.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna changamoto ya upungufu wa watalaam katika huduma za afya katika vituo vyetu na Hospitali za Halmashauri ikiwemo Manyoni na Serikali imeendelea kuomba na kutoa vibali bvya ajira na katika mwaka huu wa fedha tumeomba vibali vya watumishi 12,000 lakini kipindi hiki tunaendelea na mchakato wa kuajiri watumishi 2,796 wa kada mbalimbali za afya. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Manyoni pia itapewa kipaumbele cha kupata watumishi hawa wa afya.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa ajili ya majibu ya Naibu Waziri. Maswali mawili ya nyongeza; nini commitment ya Serikali kuhusu tabia ya kuzichelewesha fedha na baada ya muda mfupi kuzirejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili…

SPIKA: Rudia la kwanza.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Nini commitment ya Serikali kuzichelewesha fedha kuzipeleka Halmashauri na baada ya muda mfupi kuzirejesha?

SPIKA: Swali lako halisomeki, la pili na la mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Je, halmashauri itakuwa…

SPIKA: Aah! Umechelewesha unarejeshaje tena ulichokichelewesha.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: mfumo unazichukua zile fedha…

SPIKA: Naam.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Kwamba inachelewesha kutuma fedha mpaka mwezi wa tano au wa nne lakini baada ya muda mfupi tu mfumo unazirejesha kwenda Hazina kabla zile fedha hazijatumika.

Nini commitment ya Serikali… (Makofi)

SPIKA: Rudia mara ya mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Swali la mwisho je Halmashauri…

SPIKA: Hilohilo hujaeleweka

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Sijaeleweka, nasema hivi…

SPIKA: Unajua anatoka Shinyanga ni Msukuma huyu sasa inakuwa tabu kidogo.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Nini commitment ya Serikali kuhusu suala la kuchelewesha fedha kuzituma katika halmashauri husika na baada ya muda mfupi kuzirejesha kupitia huo mfumo?

SPIKA: Yaani anachosema hela inacheleweshwa kupelekwa kwenye halmashauri hadi kwenye mwezi wa nne/ tano si bajeti inaisha mwezi wa sita halafu wakishazituma kwenye halmashauri mwezi ule wa nne/tano baada ya wiki mbili/tatu wanazichukua tena fedha zilezile ndicho anachojaribu kukieleza. (Makofi)

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa elaboration.

SPIKA: La mwisho.

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, la mwisho; je, halmashauri itakuwa inatenda kosa ikizikatalia zile fedha zisirejeshwe kwenye mfumo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Bajeti Na. 11 ya mwaka 2015 inaeleza vizuri utaratibu wa fedha zinazopelekwa kwenye mamlaka za Serikali za Mitaa ambazo zimepangiwa majukumu mahususi lakini hazitatumika mpaka tarehe 30 Juni ya mwaka husika wa fedha.

Utaratibu uliolekezwa na sheria ni kwamba Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wakishaona fedha zimeingia kwa kuchelewa na kwa mazingira halisi hawawezi kuzitekelezea majukumu yake by tarehe 30 Juni ya mwaka husika wanatakiwa kuandika barua kwa Katibu Mkuu Hazina kupitia Katibu Mkuu TAMISEMI kuomba maombi maalum na kutoa sababu za msingi kwamba fedha zile hazitaweza kutumika kwa tarehe husika na hivyo wapewe kibali maalum cha kutumia fedha zile ndani ya robo ya kwanza ya mwaka wa fedha unaofuata kwa maana ya Julai, Agosti na Septemba ya mwaka wa fedha unaofuata.

Mheshimiwa Spika, changamoto iliyopo, Wakurugenzi wengi wamekuwa hawaitekelezi ipasavyo sheria hiyo na nichukue nafasi hii kutoa wito na maelekezo kwa Wakurugenzi wa halmashauri kwanza kuhakikisha wanaongeza kasi ya utekelezaji wa miradi mara wanapopokea fedha lakini pili kutekeleza sheria hiyo kwa kuomba kibali maalum cha matumizi ya fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, pili; mifumo ambayo kimsingi inatumika katika kupeleka hizi fedha na kutumia katika mazingira hayo zina changamoto zake lakini Serikali inaendelea kuboresha kuhakikisha karibu na mwisho wa mwaka mifumo hii inafanya kazi na kuwezesha miradi ya maendeleo kutekelezwa.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba Mheshimiwa Naibu Waziri anisaidie kujibu, hicho kituo cha afya kipo mbali sana, kimejitenga ndio kila siku napigia kelele habari za barabara. Atuambie ni lini sasa Serikali itapatia kituo cha afya pale gari ya kubebea wagonjwa kwa sababu ipo mbali sana, ni tofauti na maeneo mengine anayosema?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kituo cha afya ambacho gari hilo linatoa huduma kipo mbali na kituo hiki ambacho kinahitaji gari lingine la nyongeza kwa ajili ya kusaidia gari dogo lililopo. Kwa kutambua hilo, Serikali imeona ni busara gari lile liwe standby wakati wowote kusaidia ikitokea kuna dharura pamoja na umbali wakati tunaendelea kutafuta fedha, Serikali kwa kushirikiana na wadau ili tuweze kupata gari kwa ajili ya kuhakikisha linapelekwa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge jukumu ambalo limechukuliwa na Serikali ni la muda mfupi la kuondoa changamoto ya kukosa magari ya wagonjwa, lakini mpango ni kutafuta fedha na nikuhakikishie kwamba fedha zikipatikana, tukipata magari ya wagonjwa tutakupa kipaumbele katika Jimbo la Mufindi Kusini.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali; kwa kuwa tulishawahi kupata mafanikio katika kuunganisha baadhi ya shughuli za taasisi fulani kwa mfano tuliunganisha TRL pamoja na RAHCO, lakini pia kwa ufanisi kabisa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imeweza kuunganishwa.

Je, Serikali haioni sasa kwamba imefika mahali kwamba tulete mabadiliko ya sheria ambayo tutaunganisha sasa TARURA pamoja na TANROADS ili waweze kufanya kazi pamoja tuweze kuondoa hii kero ambayo hii kila siku kunakuwa na mapungufu ya fedha?

Mheshimiwa Spika, Tabora Mjini ina kata 29 na vijiji visivyopungua 41, imeathirika sana pembezoni Kata za Tambuka Reli, Ntarikwa, Uyui, Ifucha na kata nyingi za pembezoni.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muda muafaka pamoja na kwamba imetenga bajeti ya nyongeza kuweza kufanya haraka kutengeneza zile barabara kwa sababu nyingine hazipitiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza niseme dhumuni la Serikali kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ilikuwa ni kuiwezesha Mamlaka hii kuwa karibu zaidi na wananchi na barabara za vijijini na mijini ili tathmini ya kina na ya haraka iweze kufanyika na kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa mapema iwezekanavyo kuliko ilivyokuwa inasimamiwa na TANROADS kutokana na ukubwa wa nchi na majukumu ambayo TANROADS ilikuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TARURA inafanya kazi yake vizuri na kwa kushikirina kwa karibu sana na TANROADS tunaendelea kuhakikisha barabara zetu za mijini na vijijini zinapitika vizuri na changamoto ya fedha haitakuwa na suluhu kama tutaunganisha TANROADS na TARURA kwa sababu Serikali ni moja na vyanzo ni vilevile. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba TARURA inafanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na suala la barabara za Tabora Mjini; ni kweli nchini kote tumepata changamoto ya uharibifu wa barabara nyingi na nimhakikishie kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tayari fedha zimetengwa zaidi ya mara moja na nusu ya fedha za mwaka wa fedha uliopita ili kuhakikisha kwamba fedha zile zinatumika kurekebisha miuondombinu mingi ya barabara na katika Jimbo la Tabora Mjini barabara Mama Onyango, Kilimbika, Jobodo, Mkoani, Lubatuka, Manolelo, Inala, Shule ya Msingi Jamhuri na nyingine tayari kazi za mrekebisho zinaendelea na nimhakikishie zitaendelea kufanyiwa marekebisho, ahsante sana. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; nilikuwa nasema kwa kuwa barabara nyingi za vijijini ambazo zinahudumiwa na TARURA zimeonekana kutokuwa na uteshelevu wa bajeti na angalau TANROADS kuonekana wana bajeti ya kutosha.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha barabara nyingi ambazo zipo vijijini zinazochelewa kupandishwa hadhi kwenda TANROADS ili angalau ziweze kusaidiwa kwa sababu barabara za vijijini tunapata shida sana na bajeti ya TARURA ni ndogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester Sichalwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, bajeti ya fedha zinazotengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Wakala wa Vijijini na Mijini imeendelea kuboreshwa mwaka hadi mwaka. Kama nilivyojibu kwenye swali la msingi katika mwaka wa fedha 2019/2020, 2020/2021 bajeti ilikuwa bilioni 275.034 lakini mwaka ujao wa fedha ni shilingi bilioni 400, ongezeko la zaidi ya shilingi bilioni 125. Jitihada hizi zote ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kuboresha uwezo wa TARURA kuhudumia barabara zetu za vijijini.

Mheshimiwa Spika, na naomba nichukue hoja yako, tutaendelea kufanya tathmini kwenye barabara hizo ambazo zinahitaji kusajiliwa wa TARURA lakini zile ambazo zinahitaji kupandishwa hadhi kwenda TANROADS kuna utaratibu ambao Serikali imeelekeza naomba tuufuate huo ili tuweze kupata barabara zenye hadhi hiyo na kufanyiwa matengenezo kwa wakati, ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante; pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, barabara hii ambayo inatoka Wilaya ya Igunga kuja Loya mpaka Magulyati ni barabara muhimu kwenye uchumi wa wananchi wa Jimbo la Igalula, lakini barabara hii ina mito zaidi ya tisa, kwa tafiti ya mkandarasi inasema kila mto mmoja kwa kujenga box culvert inagharimu takribani shilingi milioni 100. Leo Waziri ananiambia ametenga milioni 200 maana ma-box culvert mawili tu hela itakuwa imekwisha.

Je, Serikali haioni haja ya kuitilia kipaumbele kuiongezea fedha hii barabara ili wananchi waweze kupita masaa yote? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, barabara hii ina vigezo na imekidhi vigezo vya kupandishwa hadhi ihudumiwe na TANROADS kwa sababu inaunganisha Wilaya mbili ya Igunga na Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, lakini vilevile inaunganisha na Mkoa wa Tabora na Singida. Kwa nini Serikali isipitie mchakato kuipandisha hadhi iweze kuhudumiwa na TANROADS ili kuepuka bajeti ndogo ya TARURA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Venant Daudi Protas, Mbunge wa Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Igalula na barabara hii imepitiwa na mito mingi na kama ambavyo nimeongea kwenye jibu langu la msingi, Serikali imetenga zaidi ya shilingi milioni 600 katika mwaka wa fedha 2021 tunaomaliza lakini katika mwaka wa fedha unaokuja. Jumla ya shilingi milioni 600 kwa ajili ya kutambua umuhimu wa barabara hii.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie pamoja na ma-culvert ambayo tumeendelea kujenga lakini tathmini itafanyika katika maeneo mengine yote ya barabara ile ambayo yanahitaji kujengewa ma-culvert lakini pia na madaraja ili fedha iweze kutafutwa na iweze kutengwa kwa ajili ya kujenga madaraja hayo kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, barabara zote ambazo zinahitaji kupandishwa hadhi kwenda kuwa barabara za TANROADS utaratibu upo wazi unaanza katika ngazi ya Halmashauri husika DCC tunakwenda RCC na baadae unawasilishwa katika Wizara za TAMISEMI na Ujenzi.

Kwa hiyo, naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba wafuate utaratibu huo ili tuweze kuona kama inakidhi vigezo iweze kupata hadhi inayotakiwa, nashukuru sana.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri lakini nilitaka kuongeza kwenye majibu yake kwa mara ya kwanza Serikali imesikia kilio cha Waheshimiwa Wabunge kwa sababu fedha za TARURA zilikuwa zinatoka katika Mfuko wa Barabara, kwa mara ya kwanza tumepata fedha shilingi bilioni 172 kutoka Mfuko Mkuu wa Hazina. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu fedha hizi tumezipata haraka haraka na bajeti zilishapitishwa na Kamati za Halmashauri, kwa hiyo tumetumia maamuzi ya jumla kila Jimbo tunapeleka shilingi milioni 500 TARURA kwa ajili ya ujenzi wa barabara. (Makofi)

Kwa hiyo, Halmashauri au Waheshimiwa Wabunge mtaamua milioni 500 kujenga kilometa moja ya barabara ya lami au milioni hiyo 500 kujenga kilometa 10 kupandisha barabara ya udongo kuwa ya changarawe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeiweka hii chini ya uamuzi wa Mabaraza ya Madiwani kuamua milioni hii 500 kwa kila Jimbo sio kwa kila Halmashauri. Kwa hiyo, kama Halmashauri ina Majimbo matatu kila Halmashauri itapata milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa barabara. Na hii ndiyo kazi ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amesikia kilio chenu Waheshimiwa Wabunge na Waziri wa Fedha ananiambia bado wanaangaliaangalia kwa hiyo mambo yanaweza yakawa mazuri zaidi. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru na nishukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri, naomba nipate nafasi sasa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza ambayo kimsingi yanatokana na jibu la swali la msingi.

Swali langu la kwanza, kwa kuwa Serikali imekiri kwamba mwaka 2020/2021 kiasi cha shilingi milioni 500 kilichangwa kwa ajili ya kununua vifaa tiba, lakini sasa tumebakiza mwezi mmoja unaokuja wa sita.

Je, ni lini Serikali sasa hii milioni 500 iliyokuwa imetengwa itaweza kufika kwenye hospitali hii ili kuweza kununua vifaa tiba hivi ili kuongeza wigo wa utoaji huduma katika hospitali ile?

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, kwa kuwa Serikali imekiri mwezi Disemba mwaka huu hospitali ile itafunguliwa kwa ajili ya kutoa huduma lakini pia inakiri kwamba hatuna jengo la upasuaji na wala halijaanza kujengwa; je, jengo hili ni lini litaanza kujengwa ili itakapofika mwezi Desemba hospitali ile iweze kutoa huduma inavyotakiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo:-

Kimsingi tumetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya hospitali zote 67 za Halmashauri za awamu ya kwanza ikiwepo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya na fedha hizo tayari zimeshapelekwa Bohari Kuu ya Madawa (MSD) kwa ajili ya kununua vifaa tiba ambavyo Halmashauri ya Rorya wameainisha kwamba ni mahitaji yao ya kipaumbele.

Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha hizo tayari zimekwishatolewa kwa ajili ya Hospitali ya Rorya ana tayari zimekwishawasilishwa MSD, taratibu za manunuzi ya vifaa tiba zinakamilishwa na vifaa tiba vitaletwa katika Halmashauri ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na jengo la upasuaji; hospitali ile tayari ina majengo saba, tunaendelea na ujenzi wa majengo tisa na kati ya majengo saba ambayo tayari yamekamilika kwa asilimia 98, jengo la akina mama wajawazito linaungana na jengo la upasuaji. Kwa hiyo, tayari tuna jengo la upasuaji la kuanzia katika Hospitali ya Wilaya ya Rorya. Mpango ni kuendelea kujenga majengo mengine ya upasuaji katika mwaka wa fedha ujao, lakini hili halitaathiri kuanza kutoa huduma za upasuaji ifikapo Disemba mwaka huu 2021, ahsante sana.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri yanayotia moyo, lakini naomba niulize swali moja tu dogo la nyongeza.

Je, Serikali ipo tayari kuongeza wataalam wa afya katika Kituo cha Afya cha Ufana ambacho kipo jirani na Bashnet ili wananchi wa Bashnet wapate huduma ya afya wakati wanasubiri kujengewa kituo cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ipo tayari kuongeza watumishi katika kituo cha afya katika ajira hizi za watumishi 2,726 zilizotangazwa, ahsante sana. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Hospitali ya Kipatimu ambayo imekuwa ikiendeshwa kwa ushirikiano kati ya Serikali na taasisi ya Kanisa Katoliki imekuwa na changamoto kubwa ya mtaalam wa mashine ya x-ray. Itakumbukwa kwamba mwaka 2017 Serikali ilitumia jumla ya shilingi milioni 60 kuleta mashine ya x-ray katika hospitali ile lakini mpaka leo hatujawa na mtumishi wa kitengo hicho.

Je, katika hizi ajira chache 2,726 ambazo zimetangazwa hivi karibuni, Mheshimiwa Waziri yupo tayari kunihakikishia kwamba moja kati ya watumishi hao atapelekwa katika Hospitali ya Kipatimu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, je, Mheshimiwa Naibu Waziri au Waziri wa TAMISEMI lini atakuwa tayari kutembelea Wilaya ya Kilwa ili kutambua changamoto mbalimbali zinazowakabili watumishi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa? Ahsante.
(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali katika kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za afya, mwaka 2017 ilipeleka mashine ya x-ray na mpaka sasa utaratibu wa kumpata mtumishi kwa maana ya mtaalam wa x-ray upo hatua za mwisho na naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika ajira hizi ambazo tumezitangaza, tutakwenda kuhakikisha tunapata mtaalam wa x-ray kwa ajili ya kwenda kutoa huduma katika Hospitali ya Kipatimo.

Mheshimiwa Spika, lakini pili niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge kufanya ziara katika Jimbo la Kilwa mara baada ya kumaliza session hizi za Bunge Juni 30, 2021. Ninakushukuru sana. (Makofi)
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa tayari kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa vifaa tiba lakini pia bado kuna tatizo la ukosefu wa vyumba vya kuhudumia hawa watoto njiti katika vituo vyetu vya afya pamoja na Hospitali zetu za Wilaya.

Je, Serikali inamkakati gani katika kuhakikisha kila Hospitali yetu ya Wilaya navituo vya afya inakuwa na vyumba hivyo kwa ajili ya kuhudumia watoto hao?

Mheshimiwa Spika, swali lapili pale Mererani tuna kituo kikubwa cha afya ambacho kinahudumia kata zaidi ya nne katika Wilaya ya Simajanjiro na Wilaya za jirani kama Hai na Arusha DC, lakini tatizo kubwa lililopo pale hawana kabisa chumba maalum cha kuhifadhia maiti, hivyo ndugu zetu wanapotangulia mbele za haki ndugu wanahangaika kuwasafirisha kwenda Mount Meru na Himo.

Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kukamilisha jengo lililojengwa tayari ili huduma hiyo iweze kupatikana pale katika Kituo cha Afya cha Mererani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika ujenzi wa majengo ya huduma ya afya ya uzazi na mtoto ambayo yanaendelea nchini kote hivi sasa ramani zile zimezingatia provision ya kuwa na chumba kwa ajili ya watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao maarufu kama njiti. Kwa hiyo ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika michoro ya sasa ramani zetu zimezingatia kuwa na vyumba ambavyo vitakuwa mahsusi na vitawekewa vifaa tiba zikiwemo Radiant Warmers kwa ajili ya kusaidia watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo Serikali imeendelea pia kuhakikisha inaelimisha jamii kuhusiana na kangaroo mother care kwa maana ya huduma mwambata pamoja na kuwa vyumba hivyo. Kwa hiyo tutaendelea kuhakikisha kwamba vyumba hivyo vinakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini pili chumba cha kuhifadhia maiti katika kituo cha afya cha Mererani ni muhimu sana na mimi ninaomba tulichukue hili tutawasiliana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa maana ya Simanjiro lakini na sisi kama Serikali kuu tutaona njia bora zaidi ya kuhakikisha tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga chumba cha kuhifadhia maiti. Ninakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana, Kituo cha Afya cha Kidatu Nyandeo kina uhaba mkubwa sana wa jokofu la kuhifadhia miili ya marehemu na mara ya mwisho tuliwasiliana na MSD wakasema kwamba wangepeleka jokofu hilo lakini mpaka sasa hawajapeleka.

Je, lini Serikali itapeleka Jokofu katika Kituo cha Afya cha Nyandeo Tarafa ya Kidatu Jimbo la Kilombero?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abubakari Asenga, Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuweka mipango ya kupata vifaa tiba na vifaa mbalimbali yakiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti, lakini pamoja na jitihada za Serikali tumeendelea pia kuhakikisha tunawaelekeza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali kuona umuhimu wa kutenga fedha katika mapato ya ndani kununua baadhi ya vifaa tiba na baadhi ya vitendea kazi katika hospitali zetu yakiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba nichukue nafasi hii kumwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero kwa sababu majokofu haya ni kati ya Milioni 12 hadi Milioni 30; fedha hii ipo ndani ya uwezo wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilombero na hivyo ninamuelekeza katika mwaka ujao wa fedha wahakikishe wanaweka provision ya kununua jokofu la kuhifadhia maiti katika kituo cha afya. Nakushukuru sana.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa tayari kuna changamoto kubwa ya ukosefu wa vifaa tiba lakini pia bado kuna tatizo la ukosefu wa vyumba vya kuhudumia hawa watoto njiti katika vituo vyetu vya afya pamoja na Hospitali zetu za Wilaya.

Je, Serikali inamkakati gani katika kuhakikisha kila Hospitali yetu ya Wilaya navituo vya afya inakuwa na vyumba hivyo kwa ajili ya kuhudumia watoto hao?

Mheshimiwa Spika, swali lapili pale Mererani tuna kituo kikubwa cha afya ambacho kinahudumia kata zaidi ya nne katika Wilaya ya Simajanjiro na Wilaya za jirani kama Hai na Arusha DC, lakini tatizo kubwa lililopo pale hawana kabisa chumba maalum cha kuhifadhia maiti, hivyo ndugu zetu wanapotangulia mbele za haki ndugu wanahangaika kuwasafirisha kwenda Mount Meru na Himo.

Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya kukamilisha jengo lililojengwa tayari ili huduma hiyo iweze kupatikana pale katika Kituo cha Afya cha Mererani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika ujenzi wa majengo ya huduma ya afya ya uzazi na mtoto ambayo yanaendelea nchini kote hivi sasa ramani zile zimezingatia provision ya kuwa na chumba kwa ajili ya watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao maarufu kama njiti. Kwa hiyo ninaomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika michoro ya sasa ramani zetu zimezingatia kuwa na vyumba ambavyo vitakuwa mahsusi na vitawekewa vifaa tiba zikiwemo Radiant Warmers kwa ajili ya kusaidia watoto wanaozaliwa kabla ya muda wao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo Serikali imeendelea pia kuhakikisha inaelimisha jamii kuhusiana na kangaroo mother care kwa maana ya huduma mwambata pamoja na kuwa vyumba hivyo. Kwa hiyo tutaendelea kuhakikisha kwamba vyumba hivyo vinakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, lakini pili chumba cha kuhifadhia maiti katika kituo cha afya cha Mererani ni muhimu sana na mimi ninaomba tulichukue hili tutawasiliana na Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwa maana ya Simanjiro lakini na sisi kama Serikali kuu tutaona njia bora zaidi ya kuhakikisha tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga chumba cha kuhifadhia maiti. Ninakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru sana, Kituo cha Afya cha Kidatu Nyandeo kina uhaba mkubwa sana wa jokofu la kuhifadhia miili ya marehemu na mara ya mwisho tuliwasiliana na MSD wakasema kwamba wangepeleka jokofu hilo lakini mpaka sasa hawajapeleka.

Je, lini Serikali itapeleka Jokofu katika Kituo cha Afya cha Nyandeo Tarafa ya Kidatu Jimbo la Kilombero?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abubakari Asenga, Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuweka mipango ya kupata vifaa tiba na vifaa mbalimbali yakiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti, lakini pamoja na jitihada za Serikali tumeendelea pia kuhakikisha tunawaelekeza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali kuona umuhimu wa kutenga fedha katika mapato ya ndani kununua baadhi ya vifaa tiba na baadhi ya vitendea kazi katika hospitali zetu yakiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninaomba nichukue nafasi hii kumwagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilombero kwa sababu majokofu haya ni kati ya Milioni 12 hadi Milioni 30; fedha hii ipo ndani ya uwezo wa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilombero na hivyo ninamuelekeza katika mwaka ujao wa fedha wahakikishe wanaweka provision ya kununua jokofu la kuhifadhia maiti katika kituo cha afya. Nakushukuru sana.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba Mheshimiwa Naibu Waziri anisaidie kujibu, hicho kituo cha afya kipo mbali sana, kimejitenga ndio kila siku napigia kelele habari za barabara. Atuambie ni lini sasa Serikali itapatia kituo cha afya pale gari ya kubebea wagonjwa kwa sababu ipo mbali sana, ni tofauti na maeneo mengine anayosema?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kihenzile, Mbunge wa Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kituo cha afya ambacho gari hilo linatoa huduma kipo mbali na kituo hiki ambacho kinahitaji gari lingine la nyongeza kwa ajili ya kusaidia gari dogo lililopo. Kwa kutambua hilo, Serikali imeona ni busara gari lile liwe standby wakati wowote kusaidia ikitokea kuna dharura pamoja na umbali wakati tunaendelea kutafuta fedha, Serikali kwa kushirikiana na wadau ili tuweze kupata gari kwa ajili ya kuhakikisha linapelekwa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge jukumu ambalo limechukuliwa na Serikali ni la muda mfupi la kuondoa changamoto ya kukosa magari ya wagonjwa, lakini mpango ni kutafuta fedha na nikuhakikishie kwamba fedha zikipatikana, tukipata magari ya wagonjwa tutakupa kipaumbele katika Jimbo la Mufindi Kusini.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali; kwa kuwa tulishawahi kupata mafanikio katika kuunganisha baadhi ya shughuli za taasisi fulani kwa mfano tuliunganisha TRL pamoja na RAHCO, lakini pia kwa ufanisi kabisa Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imeweza kuunganishwa.

Je, Serikali haioni sasa kwamba imefika mahali kwamba tulete mabadiliko ya sheria ambayo tutaunganisha sasa TARURA pamoja na TANROADS ili waweze kufanya kazi pamoja tuweze kuondoa hii kero ambayo hii kila siku kunakuwa na mapungufu ya fedha?

Mheshimiwa Spika, Tabora Mjini ina kata 29 na vijiji visivyopungua 41, imeathirika sana pembezoni Kata za Tambuka Reli, Ntarikwa, Uyui, Ifucha na kata nyingi za pembezoni.

Je, Serikali haioni sasa kwamba ni muda muafaka pamoja na kwamba imetenga bajeti ya nyongeza kuweza kufanya haraka kutengeneza zile barabara kwa sababu nyingine hazipitiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza niseme dhumuni la Serikali kuanzisha Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini ilikuwa ni kuiwezesha Mamlaka hii kuwa karibu zaidi na wananchi na barabara za vijijini na mijini ili tathmini ya kina na ya haraka iweze kufanyika na kuhakikisha kwamba barabara hizi zinajengwa mapema iwezekanavyo kuliko ilivyokuwa inasimamiwa na TANROADS kutokana na ukubwa wa nchi na majukumu ambayo TANROADS ilikuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TARURA inafanya kazi yake vizuri na kwa kushikirina kwa karibu sana na TANROADS tunaendelea kuhakikisha barabara zetu za mijini na vijijini zinapitika vizuri na changamoto ya fedha haitakuwa na suluhu kama tutaunganisha TANROADS na TARURA kwa sababu Serikali ni moja na vyanzo ni vilevile. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba TARURA inafanya kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na suala la barabara za Tabora Mjini; ni kweli nchini kote tumepata changamoto ya uharibifu wa barabara nyingi na nimhakikishie kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tayari fedha zimetengwa zaidi ya mara moja na nusu ya fedha za mwaka wa fedha uliopita ili kuhakikisha kwamba fedha zile zinatumika kurekebisha miuondombinu mingi ya barabara na katika Jimbo la Tabora Mjini barabara Mama Onyango, Kilimbika, Jobodo, Mkoani, Lubatuka, Manolelo, Inala, Shule ya Msingi Jamhuri na nyingine tayari kazi za mrekebisho zinaendelea na nimhakikishie zitaendelea kufanyiwa marekebisho, ahsante sana. (Makofi)
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; nilikuwa nasema kwa kuwa barabara nyingi za vijijini ambazo zinahudumiwa na TARURA zimeonekana kutokuwa na uteshelevu wa bajeti na angalau TANROADS kuonekana wana bajeti ya kutosha.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha barabara nyingi ambazo zipo vijijini zinazochelewa kupandishwa hadhi kwenda TANROADS ili angalau ziweze kusaidiwa kwa sababu barabara za vijijini tunapata shida sana na bajeti ya TARURA ni ndogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester Sichalwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, bajeti ya fedha zinazotengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Wakala wa Vijijini na Mijini imeendelea kuboreshwa mwaka hadi mwaka. Kama nilivyojibu kwenye swali la msingi katika mwaka wa fedha 2019/2020, 2020/2021 bajeti ilikuwa bilioni 275.034 lakini mwaka ujao wa fedha ni shilingi bilioni 400, ongezeko la zaidi ya shilingi bilioni 125. Jitihada hizi zote ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kuboresha uwezo wa TARURA kuhudumia barabara zetu za vijijini.

Mheshimiwa Spika, na naomba nichukue hoja yako, tutaendelea kufanya tathmini kwenye barabara hizo ambazo zinahitaji kusajiliwa wa TARURA lakini zile ambazo zinahitaji kupandishwa hadhi kwenda TANROADS kuna utaratibu ambao Serikali imeelekeza naomba tuufuate huo ili tuweze kupata barabara zenye hadhi hiyo na kufanyiwa matengenezo kwa wakati, ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante; pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, barabara hii ambayo inatoka Wilaya ya Igunga kuja Loya mpaka Magulyati ni barabara muhimu kwenye uchumi wa wananchi wa Jimbo la Igalula, lakini barabara hii ina mito zaidi ya tisa, kwa tafiti ya mkandarasi inasema kila mto mmoja kwa kujenga box culvert inagharimu takribani shilingi milioni 100. Leo Waziri ananiambia ametenga milioni 200 maana ma-box culvert mawili tu hela itakuwa imekwisha.

Je, Serikali haioni haja ya kuitilia kipaumbele kuiongezea fedha hii barabara ili wananchi waweze kupita masaa yote? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, barabara hii ina vigezo na imekidhi vigezo vya kupandishwa hadhi ihudumiwe na TANROADS kwa sababu inaunganisha Wilaya mbili ya Igunga na Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, lakini vilevile inaunganisha na Mkoa wa Tabora na Singida. Kwa nini Serikali isipitie mchakato kuipandisha hadhi iweze kuhudumiwa na TANROADS ili kuepuka bajeti ndogo ya TARURA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Venant Daudi Protas, Mbunge wa Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi wa wananchi wa Igalula na barabara hii imepitiwa na mito mingi na kama ambavyo nimeongea kwenye jibu langu la msingi, Serikali imetenga zaidi ya shilingi milioni 600 katika mwaka wa fedha 2021 tunaomaliza lakini katika mwaka wa fedha unaokuja. Jumla ya shilingi milioni 600 kwa ajili ya kutambua umuhimu wa barabara hii.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie pamoja na ma-culvert ambayo tumeendelea kujenga lakini tathmini itafanyika katika maeneo mengine yote ya barabara ile ambayo yanahitaji kujengewa ma-culvert lakini pia na madaraja ili fedha iweze kutafutwa na iweze kutengwa kwa ajili ya kujenga madaraja hayo kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, barabara zote ambazo zinahitaji kupandishwa hadhi kwenda kuwa barabara za TANROADS utaratibu upo wazi unaanza katika ngazi ya Halmashauri husika DCC tunakwenda RCC na baadae unawasilishwa katika Wizara za TAMISEMI na Ujenzi.

Kwa hiyo, naomba nimshauri Mheshimiwa Mbunge kwamba wafuate utaratibu huo ili tuweze kuona kama inakidhi vigezo iweze kupata hadhi inayotakiwa, nashukuru sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa changamoto iliyopo Jimbo la Mtwara Mjini la kukosa Hospitali ya Wilaya linafanana sana na changamoto ya Jimbo la Kilindi: Je, ni lini sasa Serikali itapeleka pesa kujenga Hospitali ya Wilaya ya Kilindi ili kuokoa maisha ya akina mama wa Kilindi na Mkoa wa Tanga kwa ujumla? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba tunajenga Hospitali za Wilaya na Halmashauri katika Halmashauri zote ambazo hazina Hospitali hizo nchini kote. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka wa fedha ujao 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya Halmashauri zote ambazo hazina Hospitali za Halmashauri na fedha hizo zitapelekwa kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hospitali hizo. Kwa hiyo, pamoja na Jimbo hili la Kilindi kwa maana ya Halmashauri ya Kilindi itatengewa fedha hizo kwa ajili ya ujenzi huo. Nakushukuru.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Kwa kuwa sisi Mkoa wa Ruvuma tuna changamoto; hatuna hospitali kubwa ya kisasa ya Mkoa wa Ruvuma; sehemu iliyopo ni ndogo sana; sasa hivi ukitaka kuongeza jengo lazima ubomoe jengo linguine:-

Je, Serikali ipo tayari kutupangia na kutujengea Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, mipango ya Serikali ni kuhakikisha kila Mkoa unajengewa Hospitali ya kisasa ya Rufaa ya Mkoa na Hospitali za Rufaa za Mkoa ambazo zimeendelea kujengwa katika mikoa mipya zipo hatua za mwisho kabisa za ukamilishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Mkoa wa Ruvuma una Hospitali ya Rufaa ya Mkoa, lakini hii ni ya siku nyingi nae neo ni dogo. Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya tutakwenda kufanya tathmini na kuona kama kuna uwezekano wa kuboresha hospitali iliyopo au kama kuna uwezekano wa kujenga hospitali nyingine mpya, tutapeleka taarifa katika Mkoa wa Ruvuma baada ya kufanya tathmini hiyo. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona na kunipa nafasi.

Katika Mkoa wa Arusha, Jimbo ambalo lina jiografia ngumu sana, ni Jimbo la Ngorongoro; na ukisema uweke tu Hospitali ya Wilaya pale Loliondo Mjini, Kata nyingine zenye umbali mkubwa hawawezi kupata hii huduma:-

Je, Serikali inalitizamaje Jimbo hili ili wale wananchi waweze kupata huduma nzuri za afya na zinazotakiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, ni kweli kwamba Jimbo la Ngorongoro ni kubwa na jiografia yake ina changamoto, lakini Serikali imeweka mpango mkakati wa kuhakikisha kwamba kwanza kupitia Sera ya Mpango wa Maendeleo ya Afya Msingi kila Kijiji kinakuwa na zahanati, lakini pia kila Kata inakuwa na kituo cha afya na Halmashauri kuwa na Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kupitia mpango huo ambao utakwenda kujenga zahanati katika kila Kijiji, lakini pia kujenga vituo vya afya katika kila Kata, tutakwenda kutatua changamoto ya ukubwa na jiografia ya Jimbo la Ngorongoro na hivyo tutahakikisha kwamba huduma za afya zinawafikia ipasavyo wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; katika majibu haya, inaonesha kwamba maelekezo katika Ofisi ya Mkuu wa Mkoa yametolewa tangu mwezi Februari, lakini unaweza ukaona ni miezi takribani minne lakini hakuna hatua ya majibu ama ya utekelezaji juu ya suala hili la mgogoro.

Je, Serikali ipo tayari kuhakikisha kwamba inaweka msukumo wa haraka ili mradi utatuzi huu uweze kufanyika haraka na wananchi waendelee na majukumu yao kama kawaida? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kuambatana na mimi ili kwa pamoja tuweze kwenda kuona maeneo ya mipaka na kuona njia bora ya kuweza kutatua tatizo hili kwa haraka? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Butondo kwamba mwezi Februari ni kipindi ambacho Kamati Maalum ya Wataalam ilipoundwa na Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa kwa ajili ya kufanya tathmini na kuangalia chanzo na pia kupendekeza njia muafaka za kwenda kutatua changamoto ya mgogoro kati ya vijiji hivi viwili na mwekezaji. Walipewa miezi mitatu, wameshakamilisha mwezi Mei mwaka huu, 2021, kwa hiyo, hivi sasa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga ipo katika hatua za kufanya tathmini na kutoa maelekezo ambayo yatakuwa yanaleta tija katika mgogoro huu. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba Serikali imelichukulia kwa uzito sana suala hili na inalipeleka kwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali kwa maana Ofisi ya Rais, TAMISEMI na mimi nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge mpaka kule Jimboni Kishapu ili tuweze kuona maeneo hayo na pia kwa kushirikiana na uongozi uliopo tuweze kupata suluhu ya mgogoro huo. Nakushukuru sana.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu ya Serikali, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa sasa Serikali ipo katika mchakato wa ajira hizi mpya ambazo amezitaja 6,979 hivi na sisi upungufu wetu ni walimu 1,270.

Je, haoni sasa kuna umuhimu angalau Halmashauri kama ya Lushoto ikapewa kipaumbele angalau kwa kusogeza hata kupata walimu japo 200?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa wapo walimu ambao asili yao ni Lushoto na Tanga kwa ujumla na wapo katika maeneo mbalimbali ya nchi hii na hawa wapo tayari kurudi Lushoto kuungana na wananchi wa Lushoto katika kutoa huduma hii ya elimu lakini changamoto za uhamisho ndio zinazowakwamisha.

Je, Serikali iko tayari kushirikiana na mimi kuwabaini wale wote ambao wapo tayari kurudi Lushoto ili kwenda kusaidia jukumu hili na kuondoa huu uhaba mkubwa wa walimu katika Halmashauri yetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS . TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi ni kweli kwamba katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto, lakini pia katika Jimbo la Mlalo kuna upungufu wa watumishi kwa maana ya walimu na Serikali kama ambavyo nimejibu katika jibu langu la msingi imeendelea kuwaajiri kwa awamu walimu katika Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto. Naomba nimhakikishie kwamba katika ajira hizi 6,900 ambazo zinakwenda kutolewa hivi sasa ambapo tayari taratibu za kuwa-shortlist na kuwapata walimu hao zinaendelea, tutakwenda kuhakikisha tunampa kipaumbele cha hali ya juu sana Mheshimiwa Shangazi na Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto kwa ujumla wake. Kimsingi namhakikishia kwamba tutaendelea kulifanyia kazi kwa karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; walimu wenye asili ya Lushoto ambao wanapenda kurudi kufanya kazi katika Halmashauri hiyo, utaratibu wa Serikali uko wazi na walimu na watumishi wote kote nchini wanaruhusiwa kufanya kazi sehemu yoyote, lakini wale ambao wana sababu za msingi za kuomba kurudi katika Halmashauri yoyote ile ikiwemo Lushoto bila kujali wanatokea ama hawatokei Lushoto wanaruhusiwa kufuata taratibu za Serikali za kuomba uhamisho na sisi kama Serikali tuna vigezo ambavyo tutavitazama na kuona walimu wale wanapata vibali vya kuhama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kama wapo wanaohitaji tunawakaribisha, lakini kwa kufuata vigezo na taratibu zile za Serikali, nakushukuru. (Makofi)
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza fedha hizi zimekuwa zikitolewa na Halmashauri, lakini hatuoni ni namna gani zinavyorudishwa ili kuweza kukopeshwa watu wengine; je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha inaweka mkakati thabiti wa kuhakikisha kwamba hizo fedha zinavyorudi basi wapewe na watu wengine ili waweze kupatiwa mikopo hiyo na kuweza kujiendeleza katika biashara?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kutoka kwenye asilimia nne kwa wanawake, nne kwa vijana na mbili kwa walemavu kuongeza asilimia walau ziwe 15 ili kila kundi lipate asilimia tano tano? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mbunge wa Maswa Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba fedha hizi asilimia kumi ambazo zimekuwa zinatolewa kwa vikundi vya wajasiriamali katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa zimewekwa kwa mujibu wa sheria na kKanuni ili ziwe ni fedha ambazo zinazunguka kwa maana ya revolving fund. Kwa maana kila vikundi ambavyo vinakopeshwa vinapaswa kutekeleza shughuli hizo za ujasiriamali na kurejesha fedha zile ambazo zilikopwa bila riba yoyote ili ziweze kutumika pia kuwakopesha vikundi vingine na hatimaye kuendelea kuwajengea uchumi mzuri wana vikundi katika vikundi hivi vya ujasiriamali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwa na changamoto ya urejeshaji wa fedha hizi kwenye baadhi ya vikundi vya ujasiriamali vinavyokopeshwa. Na sheria ya sasa imeweka utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba tunakwenda kufungua akaunti maalum kwa ajili ya fedha hizi za mikopo ya asilimia kumi na kuhakikisha kila kikundi cha ujasiriamali kitarejesha fedha hizo na zionekane zinarejeshwa na kukopeshwa kwenye vikundi vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwaelekeza Wakurugenzi wote wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuhakikisha wanalisimamia kwa karibu sana suala la mikopo na marejesho na sisi kama Ofisi ya Rais - TAMISEMI na Serikali kwa ujumla tutakwenda kufanya kaguzi kuona fedha zilizokopeshwa zinarejeshwa na zinaendelea kukopeshwa katika vikundi vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; tumeweka asilimia kumi kutokana na mazingira ya fedha za mapato ya ndani kuwa yana majukumu mengi sana; sote tunafahamu asilimia 40 kwa ajili ya miradi ya maendeleo, asilimia 60 kwa Halmashauri za Mijini kwa ajili ya miradi ya maendeleo, lakini pia kuna shughuli zingine nyingi. Wazo hili ni zuri la kufikiria kuongeza asilimia 15 lakini tutakwenda kulifanyia tathmini na kuona kama linawezekana kutekelezwa lakini kwa sasa tunaendelea na asilimia kumi kwa sababu tumeangalia vigezo mbalimbali ili kuziwezesha Halmashauri kuendelea na shughuli zake. Nakushukuru sana.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Jimbo la Tabora Kaskazini na Tarafa mbili na kata 19 na lina kituo kimoja tu cha afya; je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za Mbunge na wananchi za kujenga vituo vya afya katika Kata za Mabama, Usagari, Chitage ikiwa ni pamoja na kukiinua hadhi kituo cha Lolangulu? Swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hospitali mpya ya Wilaya ya Uyui imevunja rekodi ya kuwapa referral wagonjwa kwenye kituo cha afya tena kwa bodaboda.

Je, Serikali lini itapeleka gari la wagonjwa la kubebea wagonjwa katika zahanati nyingine zote katika Jimbo langu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Serikali kwa kuthamini afya za wananchi wa Halmashauri ya Uyui na Jimbo la Tabora Kaskazini imepeleka fedha ndani ya miaka mitatu zaidi ya bilioni 3.4 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Vituo vya Afya vitatu ambavyo vinatoa huduma, lakini ni kweli kwamba tunahitaji gari la wagonjwa katika Hospitali ya Halmashauri na Serikali imeshaweka mipango madhubuti kabisa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ya kutafuta magari ya wagonjwa kwa ajili ya Hospitali zetu za Halmashauri lakini pia kwa ajili ya vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimhakikishe Mheshimiwa Maige kadri mipango hii inavyoendelea kutekelezwa tutahakikisha tunapata gari la wagonjwa kwa ajili ya Hospitali ya Halmashauri, lakini pia kwa ajili ya vituo vya afya, lakini tunaamini kwamba tunahitaji kuwa na vituo vya afya katika kata zetu zote kama Sera na Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi yanavyoeleza likiwemo jimbo hili la Tabora Kaskazini kwa maana ya Halmashauri ya Uyui. Naomba nimhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba kila mwaka tunaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka ujao wa fedha tumetenga fedha kwa ajili ya vituo vya afya 221, lakini tutaendelea kutenga fedha ili kuhakikisha jimbo hili pia linapata vituo vya afya.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu ina vituo vya afya vinne ambavyo vyote havina gari la wagonjwa; je, ni lini Serikali itatuletea magari ya wagonjwa kwa vituo hivyo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika jibu langu la msingi Serikali kwa kuwa imeendelea kujenga vituo vya afya kwa wingi na Hospitali za Halmashauri automatically tumekuwa na uhitaji mkubwa sana wa magari ya wagonjwa katika vituo vyetu vya afya, lakini pia katika Hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, safari ni hatua tumeanza na hatua ya ujenzi wa vituo vya afya sasa tunakwenda na hatua ya kutafuta magari ya wagonjwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mhata kwamba tutakwenda kuangalia na kukipa kipaumbele Halmashauri ya Nanyumbu ili magari ya wagonjwa yakipatikana tuweze kupata gari hilo kwa ajili huduma bora za afya katika Halmashauri ya Nanyumbu. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa kuwa Jimbo la Tunduru Kusini lina vituo vya afya vitatu kimojawapo ni kituo cha Afya Utina ambacho kinahudumia kata nne kata ya Lukumbule, Mchesi, Utina yenyewe, Tuwemacho, pamoja na Msicheo.

Je, ni lini Serikali itaboresha Kituo cha Afya Utina?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Utina ni miongoni mwa vituo ambavyo Serikali imeendelea kuvifanyia tathmini na kuona namna bora zaidi ya kukiongezea miundombinu ya majengo, lakini pia vifaa tiba kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba tayari Serikali inafanya tathmini lakini pia kutafuta fedha kwa ajili ya kukiboresha Kituo cha Afya cha Utina, ahsante sana.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa mimi Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale nilijitokea ujenzi wa kujenga nyumba ya mama na mtoto na jengo hilo tayari limeshakamilika lakini kuna mapungufu ya vifaa vya kutunzia watoto njiti yaani incubator.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kusaidia Kituo cha Afya vifaa hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa wa Nyang’hwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa kujitolea kujenga Jengo la Huduma ya Afya ya Mama na Mtoto katika Jimbo lake la Nyang’hwale, huu ni mfano mzuri sana wa kuunga mkono nguvu za Serikali katika kuboresha huduma za afya, lakini naomba nimhakikishie kwamba tunatambua kwamba tunahitaji kuwa na vifaa tiba vya kutosha katika vituo vyetu hivi zikiwemo hizi incubator kwa ajili ya kusaidia watoto wachanga na mimi naomba nimhakikishie kwamba Serikali tunalichukua hili na lipo ndani ya uwezo wetu tutalifanyia kazi ili tuweze kupata incubator kwa ajili ya kuboresha huduma za afya katika kituo cha afya hiki kilichojengwa.
MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana Hospitali Kuu ya Mkoa wa Dodoma imekuwa ikihudumia wagonjwa wengi sana hasa kutokana na kwamba idadi kubwa ya wananchi wamehamia hapa Dodoma, lakini huduma za afya katika hospitali hii haziridhishi sana kwasababu kwa mfano sasa hivi ultra sound katika huduma za kawaida, wale wagonjwa wa kawaida ultra sound haifanyi kazi kwa muda mrefu, wananchi wamekuwa wakilalamika, lakini pia vitu vingi sana vina kasoro mimi nilikuwa naomba kuuliza.

Je, ni lini Wizara hii itaweka mkakati wa kuwa wanaiangalia hospitali hii kwa karibu zaidi ili kuhakikisha inatoa huduma kama ambavyo wananchi wanataka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lucy, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mikakati na inaitekeleza mikakati ya kuhakikisha kwamba hospitali zetu zote kuanzia Hospitali za Rufaa za Mikoa, Hospitali za Halmashauri, Vituo vya Afya lakini hata Hospitali za Kanda na ya Taifa zinatekeleza utoaji huduma bora kwa wananchi kwanza kwa kuhakikisha kwamba vifaa tiba vyote vinapatikana.

Kwa hiyo ninaomba nimhakikishe kwamba Hospitali hii ya Rufaa ya Mkoa nayo ni moja ya hospitali ambazo zinasimamiwa kwa karibu na tutaendelea kuhakikisha tunasimamia kwa karibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini changamoto ya vifaa tiba kama ultra sound naomba hili nilichukue tulifanyie tathmini kwa haraka tuone kwa nini ultra sound haifanyi kazi na kama kunahitajika ultra sound mpya basi Serikali itaweka mipango mizuri ya kununua mapema iwezekanavyo ili wananchi waweze kupata huduma bora. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ili niweze kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri, lakini asilimia zinatotajwa hapa za mgao wa dawa unaokwenda katika Kituo cha Afya hiki si sawa na uhalisia uliopo kwenye eneo la tukio.

Mimi nimuombe sasa Naibu Waziri baada ya Bunge hili aje katika kituo hicho cha afya ajionee uhalisia wa mgao huo wa dawa kwa sababu wananchi bado wanahangaika. (Makofi)

(b) Mheshimiwa Spika, katika kituo hicho cha afya wananchi wamejitolea kujenga jengo la upasuaji kwa gharama zao wao wenyewe na kwamba wamekwama katika masuala ya vifaa vya madukani; bati, boriti, nondo, rangi na mambo mengine yanayohusiana na vifaa vya dukani. Kwa misingi hiyo, je, Serikali ina mpango gani wa kusaidia katika kituo hiki cha afya ili kuweza kuwawezesha wananchi hawa waweze kupata Kituo cha Afya na nguvu zao zisipotee bure? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana; naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika swali la msingi kwamba Serikali imeweka utaratibu uko wazi kwamba zahanati inapopandishwa hadhi kuwa Kituo cha Afya maombi ya Halmashauri husika yanapelekwa kwa Katibu Mkuu Afya ili kupata mgao wa dawa kwa ngazi ya kituo cha afya na si zahanati kama ilivyokuwa mwanzo.

Kwa hiyo, naomba kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Jacqueline Msongozi Ngonyani kwa kazi kubwa anayofanya kufuatilia huduma za afya katika kituo hiki cha afya, lakini nimhakikishie kwamba tumeshaelekeza Halmashauri ilete maombi hayo na tutahakikisha sasa mgao wa dawa unaendana na kituo cha afya ili wananchi wasipate changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa.

Mheshimiwa Spika, pili nipongeze sana wananchi wa Namtumbo na katika eneo hili la Msindo kwa kuchangia maendeleo ya ujenzi wa Kituo cha Afya na kuanza ujenzi wa jengo la mama na mtoto, lakini pia jengo la upasuaji. Nimhakikishie kwamba tutahakikisha na sisi kama Serikali tunakwenda kufanya tathmini na kutafuta fedha kuunga mkono nguvu za wananchi ili Kituo cha Afya kiweze kufanya kazi vizuri zaidi, ahsante sana.
MHE. MWAMTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa moja ya changamoto ambazo zinasababisha kukosekana kwa watumishi kwenye sekta yetu ya afya ni pamoja na vifo, kustaafu na ujenzi wa vituo vya afya pamoja na zahanati. Na kwa kwakuwa bado tunaendelea na ujenzi wa vituo vya afya, je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kasi ya ujenzi wa vituo vya afya inaendana na kasi ya kuajiri watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali kwa kushirikiana na wadau mwaka 2017/2020 wameajiri watumishi 12,868 na wadau hao ni kama Benjamin Mkapa, AMREF na MDH. Je, ni upi mchango wa wadau hao katika ajira kwa sekta hii ya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA(MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi ni kweli kwamba Serikali kwa kujali na kuthamini afya za wananchi imeendelea kujenga, kukarabati na kutanua vituo vya huduma za afya ili kusogeza huduma bora za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuzingatia hilo, Serikali pia imeweka mkakati wa kuhakikisha kasi ya ujenzi wa vituo vya huduma za afya kote nchini inaendana na kasi ya ajira za watumishi ili kuviwezesha vituo hivyo kuanza kutoa huduma za afya katika vituo vyote vinavyojengwa na kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndio maana katika kipindi cha mwaka 2017 hadi 2020 jumla ya watumishi takribani 12,868, wastani ya watumishi 4,200 kila mwaka wameajiriwa lakini hivi sasa Serikali inaendelea na ajira za watumishi 2,726 ambazo pia zitakwenda kupunguza upungufu wa watumishi katika vituo vyetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba tunaajiri watumishi katika vituo hivyo, ahsante sana.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa hii nafasi. Napenda kuuliza swali langu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upungufu huo wa watumishi wa afya kwenye hivi vituo kwa nini Serikali isitoe vibali maalum kwa hizi zahanati na vituo vya afya kuajiri watumishi wa kujitolea kwa kutumia mapato yao ya ndani, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA(MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua kwamba pamoja na jitihada za Serikali Kuu kuajiri watumishi katika Sekta ya Afya lakini mamlaka za Serikali za Mitaa zina wajibu pia wa kuajiri watumishi hawa kwa mikataba kupitia mapato ya ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, na hili naomba nimhakikishie kwamba Serikali ilikwishatoa kibali kwa Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kupitia zahanati, vituo vya afya na hospitali wale ambao mapato yao yanaruhusu kuajiri watumishi kwa mikataba, waajiri na Serikali imeendelea kufanya hivyo; kuna vituo vingi ambavyo vina watumishi wa mkataba wanaolipwa na Halmashauri ili kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo, naomba nimhakikishie kwamba suala hilo lipo hivyo na niwaelekeze Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa vile vituo ambavyo vina uwezo wa kuajiri watumishi wenye sifa kwa kufuata taratibu, waajiriwe kuhakikisha kwamba tunaboresha huduma za afya katika vituo vyetu, ahsante sana.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa kuwa Naibu Waziri amejibu hapa kwamba, ni Sera ya Serikali kwamba kuwe na zahanati kwa kila kijiji, lakini pia, kituo cha afya kwa kila kata. Wilaya ya Kyerwa yenye kata 24 ina zahanati tatu, yenye vijiji 99 ina zahanati 23. Ningependa kujua je, kwa wilaya ya Kyerwa hiyo sera inatekelezwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni mkakati gani Serikali ilionao kuhakikisha wananchi wa Kyerwa nao wananufaika na Sera ya Serikali ya kuwa na huduma ya afya kila kijiji, kila kata? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge. Kama ambavyo nimejibu katika maswali ya msingi kwamba, Serikali katika kipindi cha miaka mitano imejenga zahanati zaidi ya 1,200 vituo vya afya zaidi ya 488 na hospitali za halmashauri zairi ya 102, lakini mkakati huu unaendelea kutekelezwa na Halmashauri hii ya Kyerwa ni miongoni mwa halmashauri ambazo zitapewa kipaumbele kuhakikisha vijiji vyake na kata zinapata vituo vya afya ili kusogeza huduma za afya kwa wananchi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, awamu zinazofuata tutaendelea kuongeza kasi, lakini pia kuipa kipaumbele halmashauri ya Kyerwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili. Mkakati wa Serikali ni huo wa kuhakikisha kwamba, sasa kila kijiji, lakini pia kila kata na kila halmashauri inapata vituo vya huduma za afya, ili kusogeza huduma kwa wananchi. Nakushukuru.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi na niipongeze Serikali kwa juhudi madhubuti za kuboresha ujenzi wa vituo vya afya, zahanati pamoja na hospitali:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Misenyi ni wilaya ambayo ina kata 20, lakini mpaka sasa inavyo vituo vya afya viwili. Sasa ni lini zamu ya Wilaya ya Misenyi itafikiwa angalao kuongezewa vituo vya afya kwa juhudi kubwa ambazo zimekuwa zikifanywa na Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Florent Kyombo, Mbunge wa Nkenge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo hili la Nkenge na Halmashauri ya Misenyi kwa ujumla wake Serikali imeweka kipaumbele cha kuhakikisha inafanya tathmini ya maeneo ambayo yatapewa kipaumbele cha kuanza kujenga zahanati, lakini pia vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali katika mwaka ujao wa fedha imetenga kujenga vituo vya afya 121, lakini katika miaka mingine inayofuata ya fedha pia, tutahakikisha tumeweka kipaumbele cha kujenga vituo vya afya kwa hivyo, Jimbo hili la Nkenge na Halmashauri ya Misenyi pia, ni moja ya halmashauri ambazo zitapewa kipaumbele. Nashukuru.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushkuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza mawali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, wakati Mheshimiwa Rais, mama Samia Suluhu Hassan, anahutubia wanawake wiki iliyopita, aliatoa maelekezo kwenye halmshauri zetu, waweze kutoa mikopo mikubwa kwa vikundi ili kuongeza tija ya mikopo hii. Je, lini halmashauri zetu zitaanza kutekeleza maagizo haya?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wanawake wa Mkoa wa Arusha wamenituma, pmoja na makundi mengine tajwa ya vijana na walemavu, kumekuwa na urasimu mkubwa sana kupata mikopo ya halmashauri. Wanufaika hawa wanatembea umbali mrefu, kufatilia mikopo hii Halmashauri bila ya mafanikio, naomba kusikia kauli ya Serikali juu ya jambo hili, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa viti maalim kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, ni jambo la msingi sana, Mheshimiwa Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, ameelekeza na ameweka msisitizo kuhakikisha kwamba, mamlaka za Serikali za Mitaa zinatoa mikopo yenye tija kwenye vikundi vya wajasirimali, wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Ni kweli kwamba mikopo hii ambayo imekuwa inatolewa, imekuwa inatolewa kwa kiwango kidogo, ambacho hakiwakwamui wajasiriamali kutoka hatua moja kwend hatua nyengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais TAMISEMI, tumekwishatoa maelekezo kwa Wakurugenzi wa mamlaka ya Serikali za Mitaa, kuhakikisha wanatoa mikopo hiyo yenye tija, ya kuwawezesha sajasiriamali hao kujikwamua. Kwa hiyo naomba nimuhakikishie Mheshimiwa mbunge kwamba Serikali tayari inatekeleza maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais, na tumeshatoa maelekezo kwa Wakurugenzi na kazi hiyo inaendelea kuhakikisha mikopo ile inatolewa kwa kiwango kinachokubalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni kweli kwamba kwa jografia ya halmashauri zetu nyingi, kuna umbali mkubwa kati ya maeneo ambayo wajasiriamali wanafanya shughuli zao, na Makao Makuu ambapo wanahitaji kupata huduma hizi za mikopo.

Mheshimiwa mwenyekiti, tumendelea kuboresha pia maafisa mikopo katika Halmashauri, maafisa wa maendeleo ya jamii kuwafikia wajasiriamali katika maeneo yao, kuwawezesha na kuwarahisishia uwezekano wa kupata mikopo hii. Na Serikali itaendelea kuboresha mbinu hizi ili kuendelea kurahisisha upatikanaji wa mikopo.
MHE. NAPE M. NNAUYE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushkuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa pamekuwa na tatizo la matumizi ya hizi fedha za mikopo kwa maeneo mengi, na hasa maeneo mengine zimekuwa zikipelekwa kutumika kwenye maeneo yasiyo kusudiwa baada ya kukopwa.

Je, Serikali haioni wakati umefika sasa badala ya kutoa fedha, tutoe vifaa vinanyoendana na biashara husika au shughuli husika ambao inakopewa. Kwa sababu hivi vifaa tunahakika vitakwenda kufanya shughuli iliyokusudiwa, mfano, matrekta au vifaa vya uzalishaji badala ya kutoa fedha kama fedha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Nape Moses Nnauye Mbunge wa Mtama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, Serikali inatambua kuna mikopo ambayo inatolewa kwa maada ya fedha taslim kwenye vikundi, pia kuna mikopo ambayo sasa tumeboresha utaratibu wa kutoa vifaa vitakavyowawezesha wajasiriamali kutekeleza shughuli zao; Kwa hivyo wazo lake ni zuri sana. Na sisi kama Serikali tumelichukua tumeanza kulifanyia kazi, kuna vikundi ambavyo kimsingi vinahitaji vifaa, na kuna vikundi ambayo vitahitaji fedha kwa ajili ya aina ya shughuli zake, na hili nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kulitekeleza. Ahsante Mheshimiwa Mwenyekiti.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunip nafasi hii kuuliza swali la nyongeza. Kwanza niipongeze Serikali kwa kutupelea hiyo fedha shilingi bilioni moja. Nataka kujua sasa je, ni commitment gani ya Serikali kumalizia hizo fedha shilingi bilioni 1.7 ambazo zimebaki ili jengo hilo likamilike kwa kuwa wafanyakazi wa pale katika Halmashauri yangu wanafanya kazi katika mazingira magumu sana?

Swali la pili, kwa kuwa ujenzi wa Ofisi ya Mkurugenzi ni component inaenda pamoja na ujenzi wa nyumba ya watumishi ikiwemo nyumba ya Mkurugenzi na Wakuu wa Idara. Nataka kujua je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha jambo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Kwela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee pongezi zake kwa Serikali kwa kupeleka shilingi bilioni moja, lakini commitment ya Serikali tayari imetenga shilingi bilioni moja nyingine kwenye mwaka wa fedha 2021/2022 na shilingi bilioni moja tayari ipo Halmashauri ya Sumbawanga na kazi inaanza siku hii ya leo. Kwa hiyo, nimhakikishie kwa mtiririko huu, Serikali itaendelea kutenga fedha kuhakikisha tunakamilisha jengo la utawala katika Halmashauri ya Sumbawanga.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, mpango wa ujenzi wa majengo ya utawala unaenda sambamba na mipango ya ujenzi wa nyumba ya watumishi kwa maana ya Mkurugenzi na Wakuu wa Idara. Kwa hiyo, safari ni hatua nimhakikishie wakati tunaendelea na ujenzi wa jengo la utawala pia tunakwenda kuweka mipango ya kuanza ujenzi wa nyumba za Mkurugenzi na Wakuu wa Idara kwa awamu, ahsante sana.
MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wapo wafanyabiashara ambao hawalipi ushuru, wamejitoa kwenye kodi na leseni kwa kisingizio cha kukosekana kanuni za vitambulisho vya mjasiriamali.

Ni nini kauli ya Serikali juu ya upotevu wa mapato unaosababishwa na wafanyabiashara hawa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; kwa namna hali ilivyo huko site, vitambulisho hivi inaonekana kama ni hiyari, zoezi lake ni gumu na kwa wale wanaovikataa hakuna hatua yoyote ya kuwachukulia kikanuni.

Sasa ni lini Serikali itatoa kanuni hizo za vitambulisho vya mjasiriamali ili kuondoa mkanganyiko huo na kuweka bayana masharti na utaratibu wa vitambulisho hivyo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niseme kimsingi vitambulisho hivi vilitolewa kwa nia njema ya kuhakikisha wajasiriamali na
wafanyabiashara wadogo wanafanyabiashara kwa utulivu kwa kuwa na kitambulisho kinachowawezesha kutoa huduma zao za biashara bila kulipa gharama nyingine kama ilivyokuwa siku za kule nyuma.

Kwa hiyo, kanuni zimetolewa wazi kwamba kwanza ni mfanyabiashara mdogo, mwenye mzunguko wa biashara usiozidi shilingi milioni nne kwa mwaka lakini mfanyabiashara ambaye kimsingi anapatikana katika eneo husika linalofanyabiashara, lakini anaweza kufanya biashara sehemu nyingine; lakini kanuni nyingine ni kwamba kinatumika kwa miezi 12 tangu tarehe ile ya kukatwa kitambulisho kile.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa wafanyabiashara wadogo ambao hawalipii vitambulisho hivi, maana yake watakuwa tayari kulipa gharama zilizopo kisheria za kufanya biashara kwa maana ya ushuru mbalimbali na gharama zingine. Kwa hiyo, tunaendelea kuwaelimisha na walio wengi kwa kweli wanaona hii ni njia bora zaidi kwa sababu wanapata nafuu ya kulipa ushuru kila siku kwa kulipa kitambulisho kwa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Spika, pili, vitambulisho hivi ni vya hiyari, lakini elimu inaendelea kutolewa ili walio wengi waweze kuona umuhimu wake na kuvitumia, ahsante.
MHE. MIRAJI J MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake lakini katika swali langu la msingi mpango wa Serikali ni kujenga Kituo cha Afya kila Kata na katika Jimbo la Singida Mashariki tuna Kata 13 na tunacho Kituo cha Afya kimoja tu ambacho pia hakina huduma nzuri. Kwa sababu Kata hizi hazina Kituo cha Afya, naomba kujua Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Afya katika Kata zingine ikiwemo Kata za Makiungu na Ntuntu ambayo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan wakati wa kampeni? Swali la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, namshukuru sana Mheshimiwa, ni kweli ametuletea fedha kwa ajili ya kujenga hospitali ya wilaya. Fedha hizo zilirudishwa kama ambavyo tulisema baada ya kuwa mwaka wa fedha umepita. Hivi tunavyoongea zaidi ya miezi sita, fedha hizo hazipo na ujenzi umesimama. Je, ni lini sasa Serikali italeta fedha hizo ikiwemo kuleta vifaa tiba katika hospitali hiyo ili iweze kuanza kutoa huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimetangulia kutoa ufafanuzi katika majibu yangu ya msingi kwamba Sera ya Maendeleo ya Afya ya Msingi inakwenda kuboreshwa ili iwe na tija na uhalisia na ufanisi mkubwa zaidi kwa sababu tuna vijiji karibu 12,000 na mitaa karibu 16,000 na tuna kata 3,956. Kwa hivyo, tunataka kwenda kimkakati zaidi kujenga vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati ambavyo vitakuwa fully equipped na vitatoa tija zaidi badala ya kujenga kila kata na kila Kijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika jimbo lake, vituo hivi vya afya ikiwemo kituo hiki ambacho ni ahadi ya Mheshimiwa Rais lakini na vituo vile vingine vyote tutafanya tathmini na kama tutaona tija ya kuvijenga vitakwenda kujengwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie kwamba mpango huo utaendelea kutekelezwa kwa utaratibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, fedha za hospitali ya halmashauri zilizorejeshwa, kwa kipindi hicho zilirejeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti ya Mwaka 2015 lakini Serikali imeshafanya maboresho. Waheshimiwa Wabunge wote tumesikia hapa wakati wa bajeti ya Wizara ya Fedha kwamba kuanzia Mwaka ujao wa Fedha, fedha zinazopelekwa kwenye miradi ya maendeleo hazitarejeshwa baada ya tarehe 30 Juni. Kufuatia hilo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha hizo tutafanya utaratibu kuzipeleka ili kuendelea na ujenzi wa hospitali kama ulivyopangwa. (Makofi)
MHE. ASK. JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tatizo la Singida Mashariki linafanana kabisa na tatizo la Kata ya Mabwepande katika Jimbo la Kawe, ni lini sasa Serikali itamalizia ile Hospitali ya Jimbo la Kawe katika Kata ya Mabwepande?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Askofu Josephat Gwajima, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni inajenga Hospitali ya Manispaa katika eneo la Mabwepande na mwezi wa tatu tulifanya ziara pale, tulishirikiana na Mheshimiwa Mbunge, iko hatua za mwisho za ukamilishaji na tulishatoa maelekezo kupitia mapato ya ndani wahakikishe hospitali ile inaanza kufanya kazi ndani ya mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia katika mwaka ujao wa fedha tumetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya vifaatiba lakini pia kwa ajili ya kumalizia baadhi ya shughuli za ujenzi. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za Manispaa ya Kinondoni. Ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua Sera ya Afya mbali ya ujenzi wa zahanati pamoja na vituo vya afya lakini pia kuna kupandisha hadhi vituo vya afya. Hospitali ya Manyamanyama imepandishwa hadhi na kuwa hospitali ya wilaya lakini bado inapata mgao kama kituo cha afya. Ni lini sasa itapatiwa mgao wa vifaatiba na dawa kama hospitali ya wilaya kwa sababu ipo barabarani na inatoa huduma si tu kwa Wilaya ya Bunda, hata kwenye mikoa Jirani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mipango ya Serikali ni kwamba vituo vile vyote ambavyo vimepandishwa hadhi kutoka kituo cha afya kwenda kuwa hospitali kama ilivyo Hospitali ya Manyamanyama vinastahili kuwekewa bajeti kwa ngazi ya hospitali na vifaatiba lakini pia hata ikama ya watumishi. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutalifanyia kazi hilo kwa haraka iwezekanavyo ili liingie kwenye mgao wa hospitali. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru sana Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina swali moja la nyongeza. Kutokana na uhitaji mkubwa na ukuaji wa tatizo hili la stroke, kwa maana ya kupooza na uhitaji wa mazoezi tiba na utengamao: -

Je, Serikali sasa ina mpango gani kuhakikisha kwamba inaboresha vitita vya Bima ya Afya ya Taifa na Bima ya Afya ya Jamii iliyoboreshwa ili tiba hii iwe jumuishi katika bima hizi kwa ajili ya ustawi wa wananchi wetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, kumekuwa na ongezeko kubwa sana la magonjwa yasiyoambukiza ambalo linasababisha uhitaji mkubwa sana wa tiba mazoezi pamoja na huduma za utengemao. Serikali inaendelea kuboresha mpango mkakati ambao utakuja na mbinu; kwanza za kuhakikisha tunaweka mipango madhubuti ya kuzuia magonjwa yasiyoambukiza; pili, kuwa na vifaa tiba vya kutosha na wataalam katika maeneo ya magonjwa yasiyoambukiza na pia utengamao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tutakwenda kuona wazo zuri la Mheshimiwa Mbunge tuone namna gani tunakwenda kuboresha eneo la bima ya afya, lakini na CHF na huduma nyingine kuweza ku-cover huduma hizi za mazoezi tiba na utengamao. Kwa hiyo, tumelichukua wazo hilo, ni zuri sana na kwa kipindi hiki ni wakati muafaka, tutakwenda kuoifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru na nishukuru kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ni kweli TAMISEMI walituma timu ikaja kufanya mapitio lakini tokea wakati ule tayari vile vigezo vyote viwili vilivyoonekana havijafikiwa kwa maana ya idadi ya kata ziko kata 12 na idadi ya watu ambacho ni kigezo namba mbili tayari mamlaka ile ina watu zaidi ya 200,000 ni zaidi ya kigezo ilichowekwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, swali langu sasa, je, Serikali kupitia Ofisi ya Rais - TAMISEMI, wako tayari sasa kuridhia kuifanya Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nansio kuwa halmashauri ya mjini? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi kwamba kwa wakati huo wakati tadhimini inafanyika Nansio ilikuwa haijafikia vigezo vilivyokuwa vinahitajika, lakini kwa taarifa ya Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa tumeshafikia vigezo hivyo naomba tulichukue jambo hili kama Serikali tukalifanyie tathimini, lakini pia tukajiridhishe kama vigezo hivyo vimefikiwa ndipo tuweze kuona hatua zinazofuata kwa ajili ya kufanya maamuzi. Nakushukuru.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuwa Mji Mdogo wa Namanyere tulishakidhi vigezo na taarifa ziko ofisini kwenu; ni lini sasa mtachukua hatua kwa mujibu wa sheria ili na sisi tuweze kupata Halmashauri ya Mji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kimsingi taratibu za kupandisha Mamlaka za Miji Midogo kwenda kuwa Halmashauri za Miji zina utaratibu wake, lakini zina sheria yake na hivyo Serikali siku zote inafanya tathimini kuona kama vigezo vimefikiwa na baada ya hapo hatua stahiki zinachukuliwa.

Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwa taarifa aliyoitoa Serikali pia tutakwenda kupitia vigezo vya Halmashauri kwa maana ya Mji Mdogo wa Namanyere na kama umekidhi vigezo Serikali itachukua hatua kwa mujibu wa taratibu. Ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru sana kunipa nafasi hii lakini nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kutupa majibu yenye matumaini kwa Jimbo la Same Magharibi na Wilaya nzima ya Same, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa hii ni ahadi ya Waziri Mkuu kujenga Hospitali ya Wilaya ya Same na kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Same ipo katika barabara kuu inayokwenda Arusha ambapo ajali nyingi sana zinatokea na watu wote wanaopata matatizo haya wanategemea kupata huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Same na kwa kuwa eneo limeshatengwa kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Same.

Je, Serikali inapoanza kujenga hospitali mpya 43; Wilaya ya Same itapewa kipaumbele ili iweze kujengwa hospitali na kuletwa vifaa tiba pamoja na wafanyakazi wa kutosha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Sera ya Serikali ni kuwa na zahanati angalau kwa kila kijiji na kituo cha afya kila kata; na kwa kuwa katika Jimbo langu tumejenga zahanati za kutosha takribani asilimia 80 lakini hatuna wafanyakazi na hatuna vitendea kazi.

Je, Serikali ni lini itapeleka watumishi wa afya kwenye zahanati hizo ili tuache kuzifunga zianze kutumika kusaidia wananchi wa Wilaya ya Same?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa David Mathayo David kwa juhudi zake za kuhakikisha mara kwa mara anawasiliana na Serikali kuhakikisha Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Same inajengwa; na mimi nimuhakikishie Serikali itaendelea kushirikiana naye lakini na wananchi wa Same kuhakikisha katika vipaumbele hivi tunakwenda kujenga Hospitali ya Wilaya ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, hii ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na kama ilivyo ada ahadi za viongozi wetu wa Kitaifa zinapewa kipaumbele; na mimi naomba nimuhakikishie kwamba Serikali tayari imeshaainisha ahadi zote za kitaifa za viongozi wetu wa kitaifa na zinakwenda kufanyiwa kazi kwa awamu na hospitali hii ya Same ikiwemo.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, ni kweli tuna sera ya zahanati katika vijiji na vituo vya afya katika kata, lakini tumeamua kufanya mapitio ya sera ile ili tuwe na ujenzi wa zahanati kimkakati zaidi, lakini pia ujenzi wa vituo vya afya kimkakati zaidi badala ya kuwa kila kijiji na kila kata. Lakini nimhakikishie vituo hivi vyote ambayo vimejengwa Serikali inaendelea kuajiri na watumishi hao 2,726 walioajiriwa wapo ambao watapelekwa Same na katika awamu nyingine za ajira tutahakikisha tunapeleka watumishi Same. Ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa wananchi wa Kijiji cha Magulilwa, Kata ya Magulilwa, Jimbo la Kalenga walishamaliza boma la kituo cha afya siku nyingi sana; je, ni lini Serikali itatukamilishia ujenzi wa boma hilo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, likiwemo boma hili la Magulilwa la kituo cha afya na maboma mengine yote ya vituo vya afya na zahanati, Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumefanya tathmini na kuorodhesha maboma yote na mpaka tarehe 31 Mei, 2021 tulikuwa na jumla ya maboma 8,003 ambayo tunayapa kipaumbele cha kutenga fedha kwa awamu ili yakamilike. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba boma hili la Magulilwa litapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika nakuskuru. Mradi wa soko la Tarime ulikuwa uanze awali kama alivyosema February 2019 na wananchi wote waliokuwa na vibanda pale takriban 200 walibomolewa vibanda, kwa hiyo wamekuwa wakilipwa kwa muda huu wote, na majibu ya Serikali anasema utamalizika ndani ya miezi 12, na wametenda bilioni tatu tu, wakati mradi ni bilioni 8.07, ninependa kujua sasa hio bilioni 5.07 zinapatikana wapi ili ziweze kumalizika mradi huu ndani ya miezi 12 kama mlivyoonesha, maana yake mwaka wa fedha uko within that?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tuliweza kukidhi tena vigezo vya kupata stendi ya kimkakati ya Galamasara, na wananchi walikuwa wametoa takribani milioni 70 tangu mwaka 2017, ningependa kujua pia stendi hii ya kimkakati ya Galamasara ni lini inaenda kuanza na kumalizika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimwia Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko kwa juhudi zake za kuunga mkono juhudi kubwa za Mbunge wa Jimbo hilo Mheshimiwa Michael Kembaki katika kutetea wananchi wa Tarime Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili nimhakikishie kwamba Serikali imeweka mpango wa kuhakikisha miradi mkakati ukiwemo ujenzi wa soko la kisasa katika Mji wa Tarime unakamiliswa, na ndio maana katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 tumetenga bilioni tatu na Serikali itaendelea kutenga fedha hizo kuhakikisha mradi huo unakamilika; pili fedha bilioni 5.07 zitawekwa kwenye mpango ujao wa fedha kuhakikisha linakamilishwa kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili stand hii ya kimkakati pia ni miongoni mwa mipango ambao Serikali itaendelea kuitekeleza kwa awamu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, lengo la Serikali ni kuhakikisha miradi hii inakamilika na safari ni hatua, tunaanza na hatua moja tunakwenda kukamilisha hatua nyingine, ahsante sana.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, majibu ya Serikali ni mazuri hata hivyo majibu haya yanatofautiana na majibu ambayo Serikali hii ilijibu mwaka 2016. Wakati huo walisema kwamba wamesimamisha kutoa namba za maeneo ya utawala mpaka pale watakapokamilisha taratibu zote kwa maana ya kupata watendaji, ofisi na mahitaji muhimu ili kuweza kuwa na vijiji. Leo Serikali inasema kwamba endapo watakamilisha taratibu hizi ambazo zilishakamilika zaidi ya miaka kumi, sasa swali langu kwa je, endapo nitaleta hizo documents zote zinazotoka kwenye Halmashauri ya Wilaya Masasi, Serikali itachukua muda gani kuhakikisha namba za vijiji hivi zinatolewa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na migogoro mingi ya ardhi katika maeneo mbalimbali kwa sababu Serikali imekuwa inatoa namba lakini baadaye maeneo mengine yanatangazwa kuwa ni hifadhi, maeneo mengine ni mipaka kati majeshi pamoja na vijiji mfano Kijiji cha Chingulungulu ambapo kuna Hifadhi ya Misinjesi lakini Kijiji cha Ngalole ambapo wanapakana na Magereza ya Namajani, Wilaya ya Masasi. Vijiji hivi vyote vina namba na Serikali ipo pale inasema kwamba na yenyewe pia ni maeneo yao.

Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya taasisi hizi kujiridhisha kwanza kabla ya kuamua kutwaa maeneo haya ili waweze kuwalipa fidia ama yachukuliwe na Serikali? (Makofi)

Swali la pili; kulikuwa na migogoro mingi katika maeneo mbalimbali ya ardhi, kwa sababu Serikali imekuwa inatoa namba lakini baadaye maeneo mengine yanatangazwa kuwa ni hifadhi na mengine ni mipaka kati ya majeshi pamoja na vijiji, kwa mfano Kijiji cha Chingulungulu ambapo kuna Hifadhi ya Misinjesi na Kijiji cha Ngalole ambako wanapakana na Magereza ya Namajani Wilaya ya Masasi; vijiji hivi vyote vina namba na Serikali iko pale inasema kwamba na yenyewe pia ni maeneo yao.

Je, Serikali haioni sasa kuna haja ya taasisi hizi kujiridhisha kwanza kabla ya kutwaa maeneo haya ili waweze kuwalipa fidia kabla ama yachukuliwe na Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ni kweli kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameeleza, kwamba Serikali kwa kipindi kile cha mwaka 2016 kilikuwa kinafanya mapitio ya kukamilisha mfumo bora zaidi wa usajili wa maeneo mapya ya utawala. Kwa hiyo, tangazo na maelekezo yale ya Serikali yalikuwa sahihi na yalifanyika kwa wakati ule na ndiYo maana leo Serikali imetoa maelekezo kwamba sasa Halmashauri ya Ndanda pia tunaweza tukaanza utaratibu wa kusajili vijiji hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba akileta documents zinazohitajika, tutapitia taratibu husika na muda siyo mrefu sana, baada ya mamlaka kujiridhisha uhalali na vigezo vya vijiji vile, basi tutapata vijiji vile.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, mahusiano ya usajili wa vijiji; ili kiwe Kijiji ni lazima kipate Hati ambayo inatolewa na TAMISEMI. Hivi sasa vijiji vilivyosajiliwa kwa record yangu havipungui 12,319. Baada ya hapo kila Kijiji kinatakiwa kipate Cheti kutoka kwa Kamishna wa Ardhi ili kuonyesha mipaka ya Kijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kila Kijiji Tanzania lazima kiwe na vyeti viwili; Hati ya kusajiliwa, ni Mamlaka ya Utawala kwamba sasa mnaweza kuchaguana, ni Serikali kamili. Baada ya hapo inatakiwa Kijiji kipimwe ili kiweze kupata Hati, yaani Cheti kinachoonyesha sasa utawala wenu wa Serikali unamiliki ardhi kiasi gani. Kwa hiyo, hivi sasa kuna vijiji 1,557 ambavyo havijapata Hati au Vyeti vile vya Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nahisi namna ya kuondoa mgogoro huu wa Ndanda, kwanza ipatikane hiyo Hati ya kusajili Kijiji, halafu tukapime mipaka ya Kijiji kile. Siyo kweli kwamba Kijiji hakiwezi kuwa na msitu, kinaweza kuwa na msitu, lakini Cheti chenye heshima na kinachothaminiwa na kinachotakiwa kisheria ndani ya Kijiji ni Cheti cha umiliki wa ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningeomba Waheshimiwa Wabunge, tushirikiane kuhakiki kwenye vijiji vyetu kuhakikisha kila Kijiji kina vyeti viwili; kwanza, wana Hati ya kusajiliwa kama Serikali na pia vyeti vya kumiliki ardhi. Sasa ndani ya Kijiji kunaweza kuwa na mpango wa matumizi bora ya ardhi unaoonyesha misitu, makazi, kilimo na ufugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitaka kuongeza hilo, sikuwa namjibia Waziri wa Maliasili, lakini nilikuwa natoa ufafanuzi kwamba kila kijiji kinatakiwa kipimwe kipewe Cheti cha Ardhi ya Kijiji. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sawa. Mheshimiwa Waziri, tunakushukuru kwa huo ufafanuzi. Nadhani hoja ya msingi ni kwamba Kijiji kinapopewa Hati lazima kuna vigezo ambavyo inatakiwa iwe navyo, ikiwa ni pamoja na ardhi na idadi ya watu. Kwa hiyo, Maliasili sasa wakienda pale, ile ardhi ambayo inajulikana ni ya Kijiji, halafu wao wakaweka hifadhi hapo, halafu na nyie mkaja mkakipunguza ukubwa kile Kijiji, nani anakuwa amekuja kwanza kabla ya hapo? Aliyemtangulia mwenzie ni nani? (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, Maliasili hawawezi kupora ardhi kwenye vijiji, hawawezi. Kwanza Maliasili hawatoi Cheti, wala hawatoi Hati. Wao wanatengeneza GN. Msitu wa Maliasili unaweza kuwa sehemu ya ardhi ya Kijiji. Kikubwa hapa ni Hati; Cheti kinachotawala ardhi ya Kijiji, lakini ndani mle kunaweza kuwa na shughuli mbalimbali hata za kibinadamu ndani ya Kijiji.

NAIBU SPIKA: Sawa, ahsante.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, mnaweza kuwa na ardhi ya Serikali au ya watu binafsi ndani ya Kijiji, lakini Cheti cha Kijiji kinaonyesha mipaka ya utawala ya Kijiji kizima pamoja na ardhi iliyopo.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; katika Jimbo la Manyoni Mashariki hususan Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, tuna upungufu mkubwa sana wa Watendaji wa Vijiji na tayari tulishapeleka maombi ya kupata kibali cha kuajiri Watendaji wa Vijiji na Watendaji wa Kata. Je, ni lini Serikali itatupatia kibali sasa cha kuwaajiri Watendaji wa Vijiji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika Jimbo la Manyoni Mashariki tuna kilimo kikubwa sana cha korosho kwa kutumia block farming. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kusaidia kupeleka wataalam wa kilimo ili kuchochea uwekezaji huo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Pius Chaya Mbunge wa Manyoni Mashariki, lakini pia Mheshimiwa Massare Mbunge wa Manyoni Magharibi na Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe kwa kazi kubwa sana wanazozifanya kwa pamoja, kuhakikisha wananchi wa Manyoni na Singida kwa ujumla wanapata miradi ya maendeleo kwa ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tuna changamoto ya upungufu ya Watendaji wa Vijiji na Kata katika halmashauri zetu zilizo nyingi. Serikali inaitambua changamoto hii na tathimini na mpango mkakati unaendelea kuandaliwa, hatua nzuri ili tuone namna gani tunakwenda kujaza nafasi za Watendaji wa Vijiji na Kata katika maeneo yetu ili waweze kusimamia kwa ufanisi zaidi shughuli za maendeleo. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kulifanyia kazi hilo na litapatiwa ufumbuzi kwa awamu na kwa hatua stahiki.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunahitaji wataalam wa kilimo lakini pia wa kada mbalimbali. Nalo pia linafanyiwa kazi na kwa kadri ya uwezo wa Serikali na upatikanaji wa wataalam hao tutaendelea kuajiri ili wakafanye kazi hizo. Nakushukuru sana.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Binafsi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa uamuzi wa busara sana sana wa kununua magari katika halmashauri zote za Tanzania yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; ni ukweli usiopingika kwamba huduma ya ambulance ni muhimu sana katika kuwahudumia wananchi wa Tanzania. Hata hivyo, huko nyuma imejitokeza changamoto kwamba huduma ya magari haya ya ambulance yanapelekwa sehemu moja mawili, matatu wakati sehemu nyingine hakuna magari kabisa. Sasa nini mpango wa Serikali katika kuepuka hili siku za usoni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali imefanya jambo jema sana, inaenda kujenga vituo vya afya kwenye tarafa takribani nchi nzima. Je, nini mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba tarafa zote hizo pia zinapata magari ya wagonjwa kwa maana ya ambulance? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza nipokee shukrani nyingi ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitoa kwa Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na ni kweli Dhahiri, shahiri inaonyesha kazi kubwa sana ambayo Serikali yetu ya Awamu ya Sita inaifanya katika kuboresha huduma za afya katika nchi yetu kwa kasi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa tunapeleka magari ya wagonjwa katika halmashauri mbalimbali, lakini kuna vigezo ambavyo vimekuwa vikizingatiwa wakati tunapeleka magari na ndiyo maana kumekuwa na utofauti kidogo wa idadi ya magari yanayopelekwa kwenye halmashauri moja ikilinganishwa na magari yanayopelekwa kwenye halmashauri nyingine. Moja ya vigezo ni pamoja na idadi ya wananchi, wingi wa vituo vya afya, lakini pia idadi ya matukio ya magonjwa mlipuko, lakini na ajali za barabarani.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaratibu huu ni wa kisera tutaendelea kufanya hivyo, lakini jambo la msingi ni kuhakikisha halmashauri zetu zote zinapata magari ya wagonjwa angalau kutimiza majukumu hayo bila kujali wingi wa wagonjwa na kadhalika, kwa maana ya kuhakikisha kwamba huduma zinapatikana vizuri. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge jambo hili tunalizingatia na mipango yetu ni kuendelea kuboresha.

Mheshimiwa Spika, la pili, katika ujenzi wa vituo vya afya katika kila tarafa; tunahitaji kuwa na vituo vya afya vyenye magari ya wagonjwa na magari haya yataendelea kuwekwa kwenye mipango na kufikishwa kwenye vituo vya afya vinavyojengwa katika tarafa zetu kwa awamu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Pia kama nilivyotoa taarifa hapa, tuna magari mengi ya wagonjwa yanakwenda kununuliwa mwaka huu wa fedha na hivyo tutaendelea kuboresha utaratibu huo kufikisha magari hayo. Nakushukuru sana.
MHE. SELEMAN J. ZEDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niipongeze Serikali kwa kupeleka milioni 250 katika Kituo cha Afya cha Itobo ili kuboresha miundombinu ya pale, lakini nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vituo vya afya vya zamani kama Kituo cha Afya cha Itobo na Kituo cha Afya cha Bukene vinaitwa vituo vya afya, lakini kimsingi havina ile miundombinu mizuri ambayo inafaa kuitwa kituo cha afya. Unakuta kinaitwa kituo cha afya, lakini hakina maabara, hakina wodi, hakina theater, hakina X-ray. Kwa hiyo, swali langu ni kwamba je, Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari baada ya Bunge hili na kabla ya Bunge la Februari kwenda Jimboni Bukene atembelee hivi vituo vya afya vya zamani ambavyo ni tofauti kabisa na vituo vya afya vya sasa, japo tunahesabiwa kwamba tuna vituo vya afya, lakini kimsingi haviendani kabisa na hali halisi inayopaswa kuwepo kama kituo cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Suleiman Jumanne Zedi, Mbunge wa Bukene, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipokee pongezi zake kwa kazi hii kubwa ambayo imeendelea kufanywa na Serikali Awamu ya Sita, chini ya Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha tunajenga vituo vya afya ikiwemo katika Kata ya Itobo. Hata hivyo, nimhakikishie kwamba Serikali tunatambua vyema kwamba ni kweli vituo vyetu hivi bado vina upungufu wa miundombinu na ujenzi huu kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi ni wa awamu. Kwa hiyo, tuko awamu hii ya kwanza ya ujenzi wa majengo ya kuanzia, lakini awamu ya pili tutakwenda kujenga majengo mengine yakiwemo wodi, lakini na majengo mengine ya vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwahidi Mheshimiwa Zedi kwamba niko tayari, tutakubaliana baada ya Bunge hili, tupange ratiba ya kwenda kule Bukene, tupitie Vituo vya Afya vya Itobo na Bukene, tuweze kufanya tathmini na kuona mpango wa kuendeleza ili viweze kuwa na hadhi ya vituo vya afya. Ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Changamoto iliyopo Bukene ni sawasawa na changamoto iliyopo Makete katika Kituo cha Afya cha Matamba ambacho kinahudumia zaidi watu 25,000, lakini hakina jengo la mama na mtoto, hakina X-ray. Kwa hiyo, naomba Serikali iniambie ni lini italeta fedha pale Matamba ili wananchi wangu waweze kupata huduma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Matamba Makete ni kituo ambacho kinategemewa na wananchi wengi zaidi ya 25,000, lakini ni kweli kwamba kina upungufu wa miundombinu ya majengo likiwemo jengo la mama na mtoto.

Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imechukua changamoto hiyo tunatafuta fedha ili twende kujenga majengo hayo mengine kuhakikisha wananchi wa Matamba wanapata huduma za kituo cha afya kilichokamilika. Ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niulize swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa Kituo cha Afya cha Itigi ambacho kinahudumia watu wengi katika Mji wa Itigi kama hospitali, je, Serikali ni lini itapeleka X-ray katika kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahaya Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa vituo hivi vya afya unaendana na uwekaji wa vifaa tiba zikiwemo mashine hizi za X-ray na ununuzi wa mashine hizi unakwenda kwa awamu kwa kadri ya bajeti zetu. kwa hivyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunatambua kwamba Kituo cha Afya cha Itigi kina uhitaji mkubwa wa X-ray na kinahudumia wananchi wengi, hivyo tutaendelea kutafuta fedha ili tupate mashine ya X-ray kwa ajili ya kuboresha huduma za afya katika Kituo cha Afya cha Itigi. Ahsante. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Hospitali ya Halmashauri ya Busega inahudumia takribani wakazi 300,000 na hatuna kabisa X-ray inabidi wananchi wale kwenda kutafuta huduma za X-ray kwenye wilaya nyingine kama Bariadi, Bunda na Magu. Je, ni lini Serikali itaipatia X-ray Hospitali ya Halmashauri ya Busega ili iweze kuhudumia wananchi wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Hospitali hii ya Wilaya ya Busega haina mashine ya X-ray na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika vipaumbele vya kupeleka mashine za X-ray, kipaumbele cha kwanza ni kupeleka katika hospitali za halmashauri.

Kwa hiyo, kadri ambavyo tunaendelea kuweka mipango yetu tutahakikisha hospitali zote za halmashauri zinakwenda kupata X-ray na ushahidi tumeona katika fedha hizi za UVIKO tunakwenda kununua digital X-ray zaidi ya 75 kwa ajili ya hospitali zetu za wilaya ambazo hazina, lakini pia vituo vya afya ambavyo vina idadi kubwa ya wananchi. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba tutaipa kipaumbele Hospitali ya Wilaya ya Busega. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. MRISHO S. GAMBO: Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba, Wenyeviti wa Serikali za Vijiji ndio msingi wa Serikali za Mitaa katika nchi yetu, na kwamba, maelekezo mengi ya Serikali kutoka ngazi ya TAMISEMI, mikoa, wilaya na halmashauri yanapelekwa ngazi za chini na wao ndio wanazisimamia.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, Jiji letu la Arusha limeongoza kwa mapato kwenye hii robo ya kwanza. Na ukizingatia kwamba, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/ 2022 tulitenga fedha kwa ajili ya kulipa shilingi elfu 50 kwa kila Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa na bado halmashauri yetu haifanyi hivyo. Je, ni nini kauli ya Serikali kwa Halmashauri ya Jiji la Arusha kuhusiana na changamoto hii ambayo inawakumba Wenyeviti wa halmashauri?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; ukizingatia kwamba, uchaguzi wa Serikali za Mitaa ulifanyika mwaka 2019 na mpaka sasa Wenyeviti wa Serikali za mitaa hawajapatiwa semina, hawapewi stationaries zozote, hawajapewa vitambulisho na hata bendera kwenye maeneo yao pia hazijapatikana na hasa ukizingatia pia hawana hata ofisi. Inabidi wachangishe kwa watu waende wakaombe hela kwa wadau, ili mwisho wa siku waweze kulipia ofisi.

Mheshimiwa Spika, hatuoni kwa kufanya namna hiyo tunawaweka kwanye mazingira ya rushwa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa? Je, nini kauli ya Serikali kwenye kutoa heshima kwenye ofisi za Serikali za mitaa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA, SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, viongozi hawa Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa na Vitongoji wanafanya kazi kubwa sana katika kusukuma maendeleo ya nchi yetu. Na ndio maana katika jibu la msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali imeendelea kutathmini na kuweka njia bora zaidi ya kuhakikisha tunawawezesha Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji kupata posho zao kila mwezi, lakini kwa sababu halmashauri zetu hazijawa na uwezo wa kutosha tunaendelea kuona namna gani tutaboresha mfumo huu, ili waweze kupata posho hizo.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali ilitoa mwongozo kwamba, kila halmashauri itenge fedha kulingana na uwezo wa mapato yake na iweze kuwalipa posho hizo Wenyeviti wa Mitaa.

Kwa hiyo, naomba nitoe maelekezo kwa Halmashauri ya Arusha na halmashauri nyingi zote nchini, zile ambazo zimetenga bajeti na zina uwezo wa kukusanya fedha hizo ziendelee kuwalipa Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji kwa kadiri ya bajeti ambazo wamezitenga.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, Serikali imeendelea kutoa fedha ambazo ni fidia ya vyanzo vilivyofutwa (GPG), kwa maana ya asilimia 20 kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa ofisi za vijiji na mitaa. Utaratibu huu unaendelea ili kuwezesha kuweza kununua shajara, lakini na matumizi mengine ya kila siku. Ahsante.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, katika majibu ya Serikali ambayo yametolewa na Mheshimiwa Waziri amesema kwamba, zimetengwa milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati tatu.

Je, Serikali lini itapeleka hizo fedha milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha zahanati hizo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ukamilishaji wa zahanati hizo tatu utasababisha uhitaji mkubwa wa wataalam katika kada ya afya ambapo bado mpaka muda huu tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi katika kada hiyo ya afya.

Je, lini sasa Serikali itapeleka watumishi wa kutosheleza mahitaji ya watumishi wa kada ya afya katika wilaya ya Kakonko? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ambazo zimetengwa kwenye mwaka huu wa fedha 2021/2022 zitaendelea kupelekwa kwenye majimbo yetu, kwenye kata zetu kadiri zinavyopatikana. Kwa hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, katika mwaka huu wa fedha fedha hizi zitapelekwa kwa ajili ya ujenzi wa zahanati hizi tatu katika Jimbo hili la Kakonko.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la watumishi; ujenzi wa zahanati na vituo vya afya unaenda sambamba na mipango ya ajira kwa ajili ya watumishi wetu kuhakikisha wanakwenda kutoa huduma katika vituo hivyo. Kwa hivyo, pamoja na ujenzi, lakini pia mipango ya ajira inaendelea kufanywa na vibali katika mwaka huu wa fedha vinaandaliwa kwa ajili ya kuajiri watumishi kwenda kutoa huduma za afya katika vituo hivyo. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba, suala hilo pia litakwenda sambamba na ujenzi wa vituo katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilihamasisha wananchi mbali ya kujenga shule, lakini waweze kuanza kujenga zahanati na mwisho wa siku Serikali kutoa mchango wake. Sasa wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini walihamasika sana na kwa mfano maeneo ya Zahanati ya Changuge, Mchalo, Gushigwamara, Nyamatoke, maeneo hayo yote wananchi walihamasika na nilichangia kwa kuweka fedha ya Mfuko wa Jimbo.

Je, Serikali ni lini sasa mtamalizia ili wananchi wa Jimbo la Bunda Mjini kwa maeneo ambayo nimeyataja wawe na uhakika wa kupata huduma ya afya katika maeneo yao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kujali afya za wananchi kwa kuwahamasisha kutoa nguvu zao kujenga zahanati na Serikali kuchangia nguvu za wananchi katika ukamilishaji wa maboma ya zahanati. Na katika jibu langu la msingi nimeeleza jumla ya maboma 758 yatakwenda kujengwa mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, jitihada zake, lakini pia jitihada za Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Bunda Mjini zimeendelea mara kwa mara kuikumbusha Serikali. Na nimhakikishie kwamba, tutaendelea kuhakikisha kwamba, tunatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo. ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu yaliyotolewa lakini bado kuna sintofahamu kuhusiana na status ya hiki Kituo. Nitaomba Mheshimiwa Waziri alifuatilie kwa karibu kwa sababu, wananchi wale wenye Bima wanashindwa kupata huduma kwa sababu wanasema officially hakijawa registered kwa hiyo kuna sintofahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili, pamoja na Kituo hiki lakini Njombe tuna vituo vingine viwili vya Afya ambavyo havina vifaa ambavyo tumeahidiwa kwa muda mrefu, Kituo cha Makoo pamoja na Kituo cha Kifanya. Mawaziri wametembelea pale lakini tumepewa ahadi na hatuelewi. Sasa je, Serikali inaweza ikatoa kauli kuhusiana na hivyo vituo viwili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deodatus Phillip Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Zahanati ya Ihalula imekwisha pandishwa hadhi kuwa Kituo cha Afya na imekwishapewa namba ya usajili kama Kituo cha Afya. Kwa hivyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hiyo sintofahamu ilikuwa kwa sababu hatukuwa tumepata namba rasmi ya usajili kuwa kituo cha Afya ili National Health Insurance Fund waanze kuilipa moja kwa moja. Kwa hiyo, sasa limeshafanyika, lakini kama kuna changamoto nyingine zote tutakwenda kuzifuatilia kuhakikisha wananchi wetu wanapata huduma za ngazi ya Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, tumekuwa na ujenzi wa Vituo vingi vya Afya, vikiwemo Kituo cha Afya cha Makoo na Kifanya; na mpango wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha za ununuzi wa Vifaa Tiba na Makoo ni moja ya vituo ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Nchi alitembelea, aliahidi Vifaa Tiba na utaratibu unaendelea kuhakikisha Vifaa Tiba vinafika pale. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili linafanyiwa kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nataka niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na miongozo yote ambayo ameitoa hapa swali langu lilikuwa ni ahadi ya Viongozi Wakuu, hayati Dkt. Benjamini Mkapa, Rais wa Awamu ya Tatu ambaye alikuja katika jimbo la Igalula, Kata ya Igalula mwaka 2002 na akatangaza Tarafa ya Kizenji ambapo ilikuwa na Kata Kizengi, Tula na Loya. Tulisimama kufuata miongozo hii kwa sababu Rais alikuwa kashatamka. Sasa, je kama Serikali wana utaratibu gani wa kufuatilia kauli za Rais na kuzifanyia kazi ili tusiweze kuleta mikanganyiko ya kuwa tunaomba mara mbili mbili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Jimbo la Igalula pamoja na mambo mengine ni kubwa sana na jiografia yake ni kubwa sana. Je, ni nini mkakati wa Serikali kutoa utaratibu wa kuanzisha na kutoa maagizo ya kuanzisha maeneo ya utawala mengine, maombi mapya ili tuweze kuleta hasa maombi ya halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Protas Venant, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba halmashauri ya Igalula kwa maana ya Jimbo la Igalula linahitaji kupata Tarafa ya Kizenga, lakini pamoja na maelezo ya Mheshimiwa Mbunge kwamba ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Serikali inatekeleza ahadi za viongozi wa kitaifa kwa utaratibu na kwa wakati, lakini kuna miongozo ambayo ni muhimu iweze kufuatwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na ahadi ya Mheshimiwa Rais ambayo Serikali inaitambua na tutaifanyia kazi, lakini watendaji wameelekezwa kufuata mwongozo kwa maana kuanzishwa vikao ngazi ya vijiji, kata, wilaya na mkoa ili sasa wawasilishe maombi hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kadri ya mwongozo na maamuzi yaweze kufanyika. Kwa hiyo, naomba kumhakikishia Mheshimiwa kwamba wakiwasilisha mambo hayo mamlaka husika itafanya tathmini na kufanya maamuzi kama tunaweza kuanzisha tarafa hiyo au viginevyo na taarifa rasmi zitapelekwa katika wilaya hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; utaratibu huu wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala kama nilivyotangulia kujibu kwenye swali la msingi, unaongozwa kwa miongozo ambayo ipo rasmi. Kwa hiyo kama kuna uhitaji wowote wa kuanzisha halmashauri mpya ni lazima tufuate miongozo ile. Kwa hivyo nimpe rai Mheshimiwa Mbunge na viongozi wa halmashauri husika wakafanye utaratibu wa vikao hivyo na kuleta maombi yao level ya Wizara. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, napenda kuishukuru Serikali kwa majibu mazuri ya kutelekeza ahadi hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu maana Waziri Mkuu mwenyewe alilitembelea eneo hili na aliona ufinyu wa eneo hili. Napenda pia kuishukuru Serikali kwa Waziri wa Ardhi Mheshimiwa Lukuvi kutupatia ardhi Kata ya Kiberege kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali hii ya Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa sasa hivi wakati mchakato wa ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ukiendelea Wananchi wa Halmashauri ya Mji wa Ifakara wanategemea sana kituo cha afya cha Kibaoni, kituo hiki kinakabiliwa na upungufu mkubwa sana wa watumishi.

Je, Serikali haioni kuchukua hatua za haraka kuongeza watumishi katika kituo cha afya cha Kibaoni? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kutokana na ufinyu wa ardhi na eneo la ekari takribani kumi za kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Ifakara Mjini, Ifakara Mjini mpaka sasa hivi haina Kituo cha Afya eneo lililopo ni dogo. Je, Serikali ipo tayari kutupatia ramani maalumu ya ujenzi wa ghorofa ili tufanye mchakato wa kuanza Kituo cha Afya cha Kata ya Ifakara Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee shukrani zake nyingi kwa Serikali yetu ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi ambayo imeendelea kuifanya ya kujenga vituo vya afya, hospitali na zahanati nchini kote na nimuhakikishie kwamba mpango huo ni endelevu tutaendelea kujenga vituo vya afya, zahanati, lakini na hospitali zetu za halmashauri kuhakikisha tunasogeza huduma za afya kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kituo cha afya cha Kibaoni kuwa na watumishi wachache nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ujenzi wa vituo hivi unakwenda sambamba na mipango ya kuajiri watumishi kwa awamu kwa kadri fedha zitakapopatikana, lakini pia kwa kadri ya vibali vya ajira vitakavyotolewa. Kwa hiyo, naomba nichukue suala hilo na tutakipa kipaumbele kituo cha afya cha Kibaoni ili kiweze kupata wahudumu kwenye awamu za ajira zinazofuata ili tutoe huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kituo cha afya Ifakara Mjini utaratibu upo wazi kama tunahitaji kujenga jengo la kwenda juu kwa maana ya ghorofa. Tunaomba kibali rasmi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunawasilisha michoro na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia watalaamu tunapitia na kuwashauri namna ya kujenga. Kwa hiyo tunakukaribisha kuwasilisha maombi hayo ili tuweze kuona uwezekano wa kujenga kituo hicho. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kituo cha Afya cha Mwaya – Mahenge – Ulanga majengo yake yamejengwa kwa muda mrefu na ni mabovu. Je, ni lini kitafanyiwa ukaratibu Kituo cha Afya hiki cha Mwaya? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa DKt. Christine Ishengoma Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyetu na hospitali zote za halmashauri chakavu ambazo zimejengwa muda mrefu zinaandaliwa utaratibu wa kwenda kuzifanyia ukarabati. Kwa hivyo tumeshaanza na utaratibu wa hospitali za halmashauri, tumeshazitambua hospitali 23 kongwe, lakini tutakwenda kutambua vituo afya chakavu vya siku nyingi ili tutafute fedha kwa awamu kwa ajili ya kuvifanyia ukarabati, lakini pia kuvifanyia upanuzi wa vituo vile. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishe Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati zoezi hilo linafanyika tutahakikisha pia Kituo cha Afya cha Maya kinapitiwa na kufanyiwa tathimini hiyo. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa mujibu wa muuliza swali alitaka kujua ni lini Mheshimiwa Waziri hajajibu. Sasa na naendelea kuuliza ni lindi stendi hiyo itaboreshwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, tatito lililopo katika stendi hiyo ya Bweri Musoma ni sawa kabisa na tatizo ambalo lipo katika stendi ya Mkoa katika Jimbo la Mtwara Mjini, stendi ipo eneo linaitwa Mkanaleli. Stendi ile ni mbaya sasa hivi mvua zinaponyesha maji yanatuama.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha inaboresha stendi ile iendane na viwango kama zilivyo stendi katika mikoa mingine na majimbo mengine?

Mheshimiwa Mwenyekti, nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika majibu yangu ya msingi nimesema kwamba Serikali tayari imeanza mazungumzo na Benki ya BADEA ili kupata ufadhili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi ya Bweri katika Manispaa ya Musoma Mjini, na ujenzi huo utaanza wakati wowote mara fedha hizo zitakapopatikana.

Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge wakati wowote fedha hizo zikipatikana kazi ya ujenzi wa stendi ile utaanza mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kuhusiana na stendi ya Mkanaleli naomba nimpe wito Mheshimiwa Mbunge lakini pia niwaelekeze Mamlaka za Serikali za Mitaa kwamba, miundombinu hii yote stendi lakini na miundombinu mingine ipo chini ya Mamlaka za Serikali za Mitaa, wanawajibika kuhakikisha wanatenga bajeti kujenga au kukarabati stendi hizo lakini kama uwezo wa kibajeti hautoshelezi kutenga bajeti hizo basi wanaelekezwa kuandaa maandiko maalum kwa maana ya maandiko ya kimkakati ili kuweza kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa stendi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nitoe wito kwa halmashauri hiyo kuhakikisha wanafanya tathmini mara moja ya uhitaji wa ujenzi wa stendi hiyo na kuona uwezo wao wa kuijenga lakini kuomba miradi ya kimkakati ili Serikali iweze kusaidia kujenga stendi hizo. Ahsante.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza niishukuru Serikali ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuweza kutekeleza ahadi za Viongozi wa Kitaifa hasa ilikuwa ni ahadi ya kipindi cha kampeni 2020.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu nipende tu kuuliza kulikuwa na ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa amekuja pale Chomachankola. Nilikuwa naomba pia kuweza kupata jibu juu ya Kituo cha Afya cha Chomachamkola ambacho Mheshimiwa Waziri Mkuu alituahidi kutupatia fedha kwa ajili ya kujenga majengo ya wazazi pale. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Seif Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Seif Gulamali kwa kuwasemea kwa dhati kabisa wananchi wa Jimbo la Manonga na ufuatiliaji wake kuhakikisha Serikali inaendelea kuwaletea maendeleo wananchi wa jimbo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nipokee shukrani zake nyingi kwa Serikali na kwa kweli sisi sote Waheshimiwa Wabunge tumeona kazi kubwa sana inayofanywa na Serikali katika kuboresha miundombinu ya huduma za afya na ndani ya hii miezi sita Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan amepeleka zaidi ya bilioni 58 na milioni 250 kujenga Vituo vya Afya 233 kote Nchini. Kwa hivyo, tunapokea shukrani hizi na tuwahakikishie kwamba tutaendelea kushirikiana naye kuhakikisha tunaendelea kuboresha miundombinu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la Kituo cha Afya ambacho ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, naomba nimuhakikishie kwamba ahadi zote za Viongozi wetu wa Kitaifa zinapewa kipaumbele ikiwemo kituo hiki cha Afya tutaendelea kutafuta fedha na mara zikipatikana tutakwenda kuhakikisha kwamba tunaanza ujenzi wa Kituo cha Afya hicho. Ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, matatizo yaliyopo katika Jimbo la Manonga ni sawa kabisa na matatizo yaliyopo kwenye Jimbo la Geita. Kata ya Nkome ina zahanati ambayo kwa mwezi inazalisha watoto wasiopungua 400 na Mheshimiwa Naibu Waziri amefika pale Silinde. Mheshimiwa Waziri juzi tu tumefika ukajionea hali halisi chumba kidogo ukakuta kinamama zaidi ya wanne wanajifungua pale. Sasa nimeshauliza humu mara mbili mara tatu ninapata tu ahadi ambazo hazijatekelezeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kupata majibu ya uhakika kwamba ni lini sasa kwa kuwa Mawaziri wote wamefika pale mtanipa fedha ya dharula ili niweze kuwaokoa wale wananchi wa Kata ya Nkome? Ahsante sana.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijajibu swali la Mheshimiwa Musukuma, kwanza naomba unipe nafasi nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa imani yake kwangu, kwa kunipa majukumu ya kumsaidia katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Rais wetu kwamba, kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu nitatumia maarifa na jitihada zote na kwa ushirikiano wa Waheshimiwa Wabunge naamini mtanipa ushirikiano ili nisiweze kumwangusha Mheshimiwa Rais wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Musukuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli siku si nyingi niliambatana na Mheshimiwa Musukuma kwenda kwenye Jimbo lake la Geita Vijijini. Kwanza nitumie nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Musukuma kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwatetea wananchi wake wa Geita Vijijini. Kama nilivyomuahidi Mheshimiwa Musukuma tukiwa Geita Vijijini, muda wowote Serikali tukipata fedha tutaangalia namna ya kuboresha Zahanati ya Nkome ili iweze kuwa Kituo cha Afya ili wananchi wa Kata Nkome pamoja na maeneo ya jirani waweze kupata huduma nzuri kwa mujibu wa Sera ya Kituo cha Afya. Nashukuru.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyonge kwanza niipongeze Serikali kwa kutupatia watumishi 20 kwa mwaka wa fedha 2021/2022 watumishi watatu kituo cha afya Karumwa na wanne kituo cha afya Nyang’ahwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023 kutokana na upungufu uliopo katika vituo vyetu vya Nyang’gwale ambavyo sasa hivi wilaya hiyo imekuwa na mfumuko mkubwa wa madini na watu wengi wamejazana katika wilaya hiyo huduma bado inaitajika sana kwenye kituo cha afya kama vile wilaya Je, Serikali iko tayari kutuongezea watumishi kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita ya mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kutupatia fedha nyingi katika sekta ya afya na kuweza kukamilisha zahanat zaidi ya 10 ambazo tunatarajia kuzifungua hivi karibuni. Je, Serikali imejipanga vipi kutupatia vifaa tiba na watumishi ili tuweze kuanzisha huduma katika zahanati hizo 10.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nassor Hussein Amar Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipokee pongezi zake nyingi kwa Serikali hii inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo imefanyika katika sekta ya afya. Lakini nimuhakikishie katika mwaka huu wa fedha 2021/2022 kuna vibali vya ajira ambavyo vitatolewa ili kuajiri watumishi kwenda kupunguza upungufu wa watumishi katika vituo vyetu vya afya kote nchini vikiwepo vituo vya afya katika halmashauri na Jimbo hili la Nyang’hwale. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge Jimbo la Nyang’hwale katika vituo hivi vitapewa kipaumbele katika ajira inayokuja ili kuhakikisha tunapeleka watumishi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili ni kweli kwamba tumeendelea kujenga vituo vingi katika mamlaka ya Serikali za Mitaa na Serikali imeshafanya tathimini tunajumla ya vitu 1073 ambavyo tunatarajia ifikapo Juni mwaka huu vitakuwa vimekamilika na vitahitaji vifaa tiba, vitahitaji watumishi na tathimini imeshafanyika na maandalizi ya kupata vifaa tiba hivyo na watumishi imeshafanyika kwa hiyo iliyobakia ni suala la utekelezaji. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba vituo vyetu ambavyo vinaendelea kujengwa tayari tathimini inajulikana na kazi yakupeleka watumishi na vifaa tiba itakwenda kwa awamu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani nyingi kwa Mheshimiwa Rais wetu kwa fedha tulizopata kwa kujenga vituo vya afya Pamoja na kukarabati kituo cha kule Kirua Vunjo na Marangu headquarter. Nina swali kuhusu kituo ambacho tumeahidiwa pale OPD Himo mji mdogo wa Himo. Kituo hiki kinahudumia watu wengi sana watu zaidi ya 36 elfu lakini bahati mbaya hakina majengo ya upasuaji, mahabara na Mochwari na tulipoahidiwa hili jambo na Mheshimiwa Naibu Waziri wa afya wakati wa kampeni tulijua kwamba tutafanyika na imefanyika lakini haya majengo hayapo. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri, je, ni lini tutapata fedha kwa kujenga majengo haya ili kituo hiki sasa kiweze kutumika na kutoa huduma zote zinazostahili kwa kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei Mbunge wa jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tunavituo vingi nchini vikiwepo vituo vya Jimbo Vunjo ambavyo kwanza vinamiundombinu michache kulinganisha na huhitaji wa vituo vya afya ikiwemo majengo kama mahabara majengo ya upasuaji lakini pia upungufu wa mawodi. Kwa hiyo, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kituo cha afya cha OPD himo ni miongoni mwa vituo ambavyo tumeviahinisha na tumeviwekea mpango kazi wa kutafuta fedha ili kwenda kujenga majengo hayo ambayo yatavifanya vikamilike kuwa vituo vya afya na hatimaye viweze kutoa huduma zile ambazo zinatarajiwa. Kwa hiyo, tunatafuta fedha Mheshimiwa Mbunge na niwahakikishie kwamba fedha ikipatikana tutawapa kipaumbele kitu cha afya cha OPD Himo.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hali ilivyo maeneo ya Jimbo la Nyang’hwale inafanana na kabisa na hali ilivyo kwenye Jimbo la Sumve ambalo lina Kituo cha Afya cha Nyambiti ambacho kilibadilishwa kilikuwa zahanati na kituo hicho cha afya kina hudumia kata 13 za Jimbo la Sumve ambazo zina wakazi zaidi ya laki mbili na kituo kile hakina majengo kama ya upasuaji mahabara na majengo ya muhimu ambayo yangesaidia katika kutoa huduma stahiki ya afya kwa watu wale. Je, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha watu wa Jimbo la Sumve katika kituo cha afya cha nyambiti na wenyewe wanapata huduma nzuri kama ilivyo katika vituo vingine vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasalali Mageni Mbunge wa Jimbo la Sumve kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ujumla katika halmashauri zetu na katika majimbo yetu tuna vituo vya afya ambavyo vina majengo pungufu kama nilivyotangulia kujibu katika jibu langu lililopita na mpango wa Serikali ni kuhakikisha standard ya vituo vya afya inafikiwa kwa maana ya kuwa na majengo yale yote ya muhimu yanayofanya kituo kile kiwe na hadhi ya kuwa kituo cha afya. Kwa hiyo, kuwepo kituo hiki cha afya cha Nyambiti katika jimbo hili Mheshimiwa Mbunge naomba nimuhakikishie kwamba tutafanya tathimini pia kuona umetupa taarifa kwamba hakuna majengo ya upasuaji na mahabara na tunajua ni muhimu na yanahudumia zaidi ya kata 13 ni moja ya kituo cha afya cha kimkakati na ninajua ulikihainisha kwa hiyo tukitafuta fedha tutahakikisha tunaipa kipaumbele kujenga majengo hayo ili wananchi wale wote wapate huduma bora za kituo cha afya.
MHE. ELIBARIKI I. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ambazo zimekuwa zikitolewa na Serikali kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa maboma fedha nyingi zimeonekana zimeshindwa kuyakamilisha maboma yaani kiwango cha shilingi milioni 50 zinakwenda kwenye vijiji lakini maboma hayaishi.

Je, Serikali imefanya tathmini ya kina kujua kwamba level ya maboma iliyofikiwa kwa nguvu za wananchi inahitaji fedha kiasi gani ili kumaliza maboma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ninaomba kumuuliza Waziri ni lini sasa Serikali itapeleka watumishi katika zahanati ambazo zimetengewa fedha na kukamilika ili kuhakikisha wananchi wetu wote wanapata huduma katika zahanati husika katika maeneo husika? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Kingu kwa uchapakazi wake mzuri kwa kuwasemea wananchi wa Jimbo la Singida Magharibi na kwa kweli Serikali tutaendelea kumpa ushirikiano kuhakikisha wananchi wanapata miradi hiyo ya maendeleo kwa ustawi wa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi ambazo zimepelekwa kwenye ukamilishaji wa maboma ya zahanati, kila boma ambalo limefikia hatua ya lenta linatengewa shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji na tathmini ilifanyika kwa sababu ramani zile zilitolewa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI na BOQ zake zilionesha jengo likijengwa mpaka hatua ya lenta likipewa shilingi milioni 50 jengo lile linakamilishwa bila changamoto yoyote na ndiyo maana katika maboma 555 yaliyopelekewa takribani shilingi 27,750,000,000 mwaka wa fedha uliopita zaidi ya asilimia 85 ya maboma yamekamilika, yameanza kusajiliwa kwa ajili ya kuanza kutoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo tathmini ilifanyika, lakini kuna variation za kimazingira za hapa na pale ambazo nazo huwa tunazizingatia na kama inajitokeza variation kama hiyo basi tunaona namna nzuri ya kukamilisha ujenzi wa zahanati hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili ujenzi wa zahanati na vituo vya afya kwa ujumla wake unakwenda sambamba na mpango mkakati wa kuajiri watumishi ili zahanati na vituo vianze kutoa huduma na tayari Serikali tumefanya tathmini ifikapo Juni, 2022 tutakuwa na vituo 1,073 ambavyo vitakuwa vimekamlika na tumeshafanya tathmini ya mahitaji ya vifaa tiba, lakini pia na watumishi na kwa kadri ya bajeti yetu tutaendelea kupeleka watumishi ili vituo vile vianze kutoa huduma na kupunguza upungufu wa watumishi katika maeneo hayo, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime inaelemewa kwa kupokea wagonjwa wengi kutoka nje ya mji wa Tarime mathalani kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, Serengeti, Rorya na hata wakati mwingine kutoka nchi jirani ya Kenya.

Je, Serikali haioni umuhimu sasa wa kukamilisha kituo cha afya cha Kenyamanyori pamoja na zahanati ya Nyandoto ambayo imejengwa kwa nguvu za wananchi ili walau kupunguza pressure ambayo inapelekea msongamano katika hospitali ya Mji wa Tarime?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ni kuhakikisha tunajenga zahanati na vituo vya afya ili kupunguza kwanza umbali wa wananchi kupata huduma, lakini pili kupunguza msongamano kwenye hospitali za Wilaya kama ilivyo katika hospitali ya Wilaya ya Tarime.

Kwa hivyo suala hilo ni la msingi na mipango hiyo tayari imewekwa, wito ambao nautoa kwa Halmashauri ya Tarime ni kutoa kufanya tathmini ya mahitaji ya fedha zinazotakiwa kukamilisha kituo cha afya na zahanati, pili kutenga kupitia mapato ya ndani, lakini pia Serikali Kuu tunaendelea kuangalia fursa ya kupeleka fedha ili kukamilisha zahanati hizo, ahsante.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona changamoto ya Jimbo la Singida ziko sambamba kabisa na changamoto ambazo zinaikabili wilaya ya Chunya kwenye umaliziaji wa maboma; kuna boma lililojengwa kwa nguvu ya wananchi kwenye kata ya Ifumbo lina zaidi takribani miaka minne halijakamilika.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ili ukamilishaji wa boma hili kwenye kata ya Ifumbo iweze kukamilika ilihali ukijua kata hii iko mbali sana na Makao Makuu ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu la Mheshimiwa Kasaka, Mbunge wa Lupa kama ifuatavyo: -

Mheshimwia Mwenyekiti, katika ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati tumeainisha maeneo ya kimkakati, na tuliwaomba Waheshimiwa Wabunge kuwasilisha vipaumbele. Nimuombe Mheshimiwa Mbunge, kama Kituo cha Afya katika Kata ya Ifuko ni kipaumbele basi tupate taarifa hiyo rasmi ili tuweze kuweka mpango wa kuhakikisha kwamba tunakamilisha ili wananchi wapate huduma. Ahsante.
MHE VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ili na mimi niulize swali moja la nyongeza.

Je, Serikali inaweza kutuweka katika orodha vijiji vyetu vya Ulamboni, Kilangalanga, Chengena, Luhangano na Mhangazi vyenye maboma ambayo hayajaisha ili waweze kupata hizo shilingi milioni 50 waweze kumalizia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa maboma ya zahanati na vituo vya afya kote nchini unafanywa kwa fedha za Serikali Kuu pamoja na fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri. Kwa hiyo, kuna vile vituo ambavyo vitakamilishwa kwa fedha za Serikali Kuu na hivyo tumeviainisha, lakini ukitokea uhitaji tutaainisha pia vikiwemo hivi vituo vya Kilangalanga na vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nitoe wito kwamba ujenzi wa zahanati hizi ni lazima pia Halmashauri kupiti mapato yake ya ndani, kupitia asilimia 40 ya fedha za miradi ya maendeleo au asilimia 60 watenge fedha kwa ajili ya kukamilisha baadhi ya maboma, wakati Serikali Kuu pia inatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Kawawa kwamba tumelichukua hilo na tutawasiliana kuona yapi yakamilishwe kwa mapato ya ndani na yapi tutafute fedha kutoka Serikali Kuu.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo kwa Mheshimiwa Waziri.

Je, Serikali ina mpango gani wa kumailizia Kituo cha Afya cha Gidas ambacho kinahudumia si tu wananchi wa Kata ya Gidas ila pamoja na wananchi wa mipakani mwa Kondoa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati njema wiki iliyopita tulikuwa kwenye ziara jimboni kwake na tulipita katika maeneo haya ikiwepo katika Kituo cha Afya cha Gidas.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie, kama tulivyokubaliana kwamba kituo kile ni cha kimkakati, tutakwenda kutafuta fedha ili kukikamilisha ili tuweze kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Mji wa Mafinga nadhani ndiyo hospitali inayohudumia Halmashauri nyingi kuliko hospitali yoyote hapa nchini. Hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia zaidi ya Halmashauri tano ikiwepo ya Mlimba ambayo iko Mkoa wa Morogoro. Sasa kutokana na unyeti huo, na kwamba iko kando ya barabara kuu.

Je, Seikali iko tayari kuleta watumishi katika mpango wa dharura?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali ya Wilaya ya Mafinga ni kweli iko barabarani na inahudumia wananchi wengi; na hospitali zote ambazo ziko kimkakati tunaziainisha na kuziwekea mpango, kwanza wa kupeleka vifaa tiba, lakini pia kuboresha upatikanaji wa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie kwamba tutakwenda kwa utaratibu wa kawaida wa kupata watumishi kwa ajili ya hospitali ile badala ya utaratibu wa dharura, kwa sababu utaratibu wa watumishi unapatikana kupitia vibali maalum; laini tutaaipa kipaumbele Hosptali ya Mji wa Mafinga.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Je ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi katika ujenzi wa zahanati za Nsengoni, Gaisosya, Kikatiti na Samaria? Wananchi wamehangaika kuzijenga zahanati hizi kwa miaka mingi lakini hawaoni support ya Serikali.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu kweli swali la msingi, mwaka wa fedha uliopita zaidi ya shilingi 27,750,000,000 zilipelekwa ili kukamilisha maboba 555, lakini katika mwaka wa fedha huu wa 2021/2022 zaidi ya shilingi bilioni 28.2 pia zimetengwa kwa ajili ya kukamilisha maboma 564 ya zahanati.
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa barabara hii ya Iboni-Bolisa – Bobali inakabiliwa na athari za mazingira inaendelea kubomoka na kuliwa na maji ambayo yanapita katika mito hii ambapo patakwenda kujengwa vivuko na daraja. Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kulinusuru daraja hili japo kwa kuweka fedha za dharura ili isije ikapata gharama kubwa zaidi ya kujenga daraja badala ya vivuko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, barabara zetu na madaraja haya ambayo yanakabiliwa na athari za kimazingira kama mmomonyoko wa udongo kutokana na maji yote yanafanyiwa tathmini na kuandaliwa mpango kwanza wa kudhibiti madhara haya yatokanayo na athari za kimazingira, lakini pia yanatengewa fedha kwa ajili ya kujenga vivuko au madaraja kuhakikisha barabara hizi zote zinapitika vizuri.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama nilivyojibu katika jibu langu la msingi kwanza tathmini imefanyika ikiwemo ya kudhibiti mmomonyoko ili barabara ijengwe na kupitika wakati wote. Ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.

Mheshimiwa Spika, tunajua Serikali ina mkakati wa kujenga barabara na kuunganisha Mikoa lakini barabara nyingi mnazojenga hamzingatii ile mifumo ya maji kwa hiyo unakuta barabara nyingi mvua inaponyesha magari hayapiti. Mfano ni barabara ya kutoka Dodoma kupitia Mtera kwenda Iringa ni barabara muhimu sana lakini hivi ninavyozungumza mvua ikinyesha barabara haipitiki. Najua kuna ukrabati unafanywa, Je, mna mkakati gani wa kuhakikisha barabara zinapitika wakati wote kwa kuweka mifumo ya maji. Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, katika ujenzi wa barabara zetu moja ya maeneo ambayo sasa tumeweka kipaumbele, kwanza ni kuhakikisha barabara zetu kwenye designing zinaweka kipengele cha kuweka mifereji ya ku-drain maji ili kuepusha maji kukatisha katika barabara zetu na kuziathiri lakini katika maeneo ambayo madaraja au culvat zinajengwa tumeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba madaraja yanakuwa juu ili kuepusha maji kukatisha katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikiri kwamba kuna baadhi ya maeneo kulikuwa na changamoto hizo na ndiyo maana sasa designing zetu zote zimeboreshwa kuhakikisha haturudi kwenye changamoto hizo na tutaendelea kutekeleza kwa utaratibu huo. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru, nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, matatizo ya Wakurugenzi katika halmashauri mbalimbali yanakuwepo na Madiwani wanayaona na saa nyingine wanayaripoti lakini hayafanyiwi kazi mpaka mwenye Mamlaka labda Mheshimiwa Rais apite ndiyo unakuta hatua zinachukuliwa. Mheshimiwa Waziri haoni sasa ni wakati muafaka wa kuhakikisha au kutoa maelekezo kwa wale wenye dhamana wanapoletewa malalamiko kutoka kwa Watumishi au Madiwani wayafanyie kazi na siyo kusubiria mpaka Mheshimiwa Rais apite ndiyo aende kutengua utenguzi wakati matatizo yalikuwa yanaonekana siku nyingi na Mkurugenzi pale ameleta athari kubwa katika ujenzi wa Taifa?Ninakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa taratibu za utumishi wa umma, mamlaka za nidhamu za wakurugenzi ziko katika ngazi tofauti, kama nilivyotangulia kusema, ngazi ya Katibu Mkuu Kiongozi, lakini pia Waziri mwenye dhamana. Lakini Waheshimiwa Madiwani wana nafasi na mamlaka ya kutoa taarifa ya changamoto ambazo mkurugenzi anapitia katika utekelezaji wa majukumu yake.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, hatua zimekuwa zinachukuliwa kwa wakati, lakini kuchukua hatua ni mchakato kwa sababu, kuna taratibu za uchunguzi, lakini pia kujiridhisha na yale mapungufu yanayoripotiwa kwa mkurugenzi husika, ili kuweza kutenda haki. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba, Serikali itaendelea kufuata taratibu hizo, kufanya uchunguzi kwa wakati, lakini pia, kuchukua hatua ili kutenda haki. Na kuhakikisha kwamba, halmashauri zetu zinakwenda vizuri. Ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi: -

Mheshimiwa Spika, yapata zaidi ya mwaka mmoja sasa mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Madiwani, hawakuweza kupata semina kwa ajili ya kuwajengea uwezo. Je, Serikali haioni kuwa ni wakati muafaka sasa wa kutoa semina kwa Waheshimiwa Madiwani kote nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia Issaay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Serikali kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa mara baada ya Madiwani kuchaguliwa katika mwaka 2020, maelekezo yalitolewa wakurugenzi kuhakikisha Madiwani wanapewa mafunzo kwa taratibu ambazo walijipangia wao katika halmashauri husika. Na mpaka sasa Madiwani wengi wamepata mafunzo, lakini ni kweli kuna baadhi ya halmashauri hazijafanya mafunzo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kusisitiza kwamba, halmashauri zifanye mipangilio ya ndani ya halmashauri kuhakikisha kwamba, Madiwani wanapata mafunzo hayo, lakini pia, kushirikiana na chuo chetu cha Hombolo cha mafunzo ya Local Government, ili kuhakikisha Madiwani wetu wanajua majukumu yao na mipaka yao ili kuboresha utendaji.

Kwa hiyo, jambo hilo ni endelevu litaendelea kufanyika katika ngazi ya halmashauri, ili kuhakikisha kwamba, utumishi unakwenda vizuri. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, la kwanza; baada ya ujenzi wa Kituo cha Afya Bassotu, Endasak na Gisambalay kukamilika bado tutakuwa na upungufu wa vituo vya afya 25 kwenye Wilaya ya Hanang’. Je, Serikali iko tayari kutufanyia upendeleo mahususi, ili tupate vituo vya afya viwili kwenye bajeti hii tunayoenda kuianza ya 2022/2023?

Mheshimiwa Spika, lakini la pili; Serikali imetupatia fedha milioni 300 kwa ajili ya kujenga jengo la magonjwa ya dharura kwenye hospitali ya wilaya, lakini wananchi pia, wamehamasishana tumechanga vifaa vinavyokaribia milioni 200. Je, bado tuna upungufu mkubwa wa majengo; Serikali iko tayari kutupatia fedha ili tujenge jengo la wodi kwa ajili ya wanaume? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Hanang’, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Hhayuma kwa kazi kubwa anayoifanya ya kufuatilia ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya kwa ajili ya Jimbo la Hanang’ na nimhakikishie kwamba, Serikali tutaendelea kushirikiana nae kuhakikisha wananchi wa Hanang’ wanapata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Spika, upungufu wa vituo vya afya hivi sasa tumeweka mkakati badala ya kujenga kituo cha afya kila kata, tuna kata zaidi ya 3,500 kwa hivyo, kwa sasa tunajenga vituo vya afya vya kimkakati kwenye tarafa, lakini pia kwenye kata zile ambazo zina uhitaji mkubwa kwa maana ya idadi kubwa ya wananchi, umbali mrefu zaidi kutoka kwenye kituo cha karibu, lakini na idadi ya magonjwa.

Mheshimiwa Spiika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutafanya tathmini ya mazingira yale ambayo kimsingi pale Hanang’ tunaweza kujenga vituo vya afya ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, pili; ni kweli Serikali yetu imefanya kazi kubwa ya kupeleka fedha ya ujenzi wa miundombinu ya majengo ya dharura, ikiwepo Hanang’ wamepata milioni 300 na kazi ya ujenzi wa wodi na miundombinu mingine tutaendelea kuitekeleza kwa awamu, ili hospitali ile ya Hanang’ iwe na miundombinu yote inayofanana na hospitali ya wilaya. Ahsante. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana nikupongeze kwa kupata nafasi hii. naomba niulize sasa swali dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, matatizo yaliyopo huko Hanang’ yanafanana kabisa na katika Halmashauri ya Itigi, ambayo ina Tarafa moja. Halmashauri ya Itigi ilikosa pesa za ujenzi vituo vya afya vya tarafa kwa sababu, ni tarafa moja, lakini ina kata 13. Je, sasa Serikali iko tayari kuiangalia kwa jicho la kipekee angalau tukapata kituo kimoja hapa karibuni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahaya Massare, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye swali la msingi; kigezo cha ujenzi wa vituo vya afya ni tarafa, lakini pia kata za kimkakati. Kwa hiyo, pamoja na kwamba, Itigi kuna tarafa moja, lakini bado wana sifa ya kupata vituo vya afya kupitia tathmini ya kata za kimkakati.

Kwa hiyo, naomba nilichukue hili na nitawsiliana na Mheshimiwa Yahaya ili tuweze kuona kata zipi za kimkakati tuzipe kipaumbele kwenye awamu zinazofuata za ujenzi wa vituo vya afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, katika majibu yake Mheshimiwa Naibu Waziri amesema kwamba, vituo vya afya vinavyojengwa ni vile vya kimkakati kwa kuangalia na idadi ya watu katika eneo husika. Swali langu; Je, ni lini Serikali itatoa kibali kwa Kituo cha Afya Solwa ambacho kina population kubwa na wananchi wamejitolea kujenga wao wenyewe kile kituo cha afya? Ni lini Serikali itatoa vibali ili kile kituo cha afya cha mkakati kiweze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa vituo vya afya unajumuisha tathmini za kitaalamu za vigezo ambavyo vinakidhi kujenga kituo cha afya. Na mara wataalamu katika halmashauri husika wakishafanya tathmini na kujiridhisha wananchi wanahamasishwa kuendelea kufanya uchangiaji na ujenzi kwa kutumia nguvu zao wakati Serikali pia inatafuta fedha kwa ajili ya kuwaunga mkono.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, Kituo cha Afya hiki cha Solwa kama kimeanza ujenzi, bila shaka wataalamu wamefanya tathmini na hakihitaji kibali cha Serikali maana wataalamu wale tayari wameshafanya tathmini na ujenzi umeanza hakuna kibali maalum ambacho kinatolewa, bali ni kuendelea na ujenzi kukamilisha na kusajili kituo ili wananchi waanze kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kuwaelimisha Ndugu zangu wananchi wa Solwa kwamba, hatuhitaji kibali, lakini tukamilishe ujenzi na kusajili kwa ajili ya kutoa huduma za afya. Ahsante.
SPIKA: Ahsante sana. Nilivyosikia neno kibali hapa nikawa natafakari, Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava ni kibali cha kufanya nini?

MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, kituo cha afya kilikuwa dispensary, wananchi wakaongeza kuwa kituo cha afya baada ya lile tamko la kika kata kuwa na kituo cha afya. Kwa hiyo, wananchi wamekwishajenga, wodi zimekamilika, OPD imekamilika, kilichobaki ni TAMISEMI kutoa go ahead ili kile kituo kiweze kufanya kazi.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri nadhani hapo umeelewa hoja yake vizuri. Karibu utoe ufafanuzi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kimsingi alichokuwa anamaanisha Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava ni kukipandisha hadhi kwa maana ya kukisajili sasa kuwa kituo cha afya na sio kibali.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaratibu uko wazi, halmashauri wanaandika barua kwenda Wizara ya Afya kupitia Katibu Mkuu Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, na tunaipandisha hadhi na kuipa namba ya usajili wa kituo cha afya. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge tutashirikiana kupata documents hizo ili tuweze kukisajili kituo hicho kianze kutoa huduma kwa wananchi kwa ngazi ya kituo cha afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza: -
Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Naibu Waziri amefika na ametembelea Jimbo la Mbulu Vijijini. Wananchi, wameshajenga vitu vitatu vya afya ambavyo viko hatua mbalimbali; cha Maretadu, Getanyamba na Gembako. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha katika vituo hivi ili kuvimalizia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge w Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Mbunge na kuwapongeza wananchi wa Mbulu kwa kazi nzuri wanayoifanya. Na wiki moja iliyopita tukiwa ziara tuliona kazi nzuri sana ya ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kazi hii ya ujenzi wa vituo vya afya inafanyika kwa nguvu za wananchi na Serikali kuchangia nguvu za wananchi kupitia aidha, mapato ya ndani ya halmashauri au fedha za Serikali Kuu. Kwa hivyo, naomba nitoe wito kwamba, Halmashauri ya Mbulu Vijijini katika bajeti zao, na bahati nzuri wana zaidi ya bilioni moja na milioni 300 kwa mwaka kwa hiyo, waanze kutenga kwa awamu fedha za kukamilisha baaadhi ya vituo vya afya ambavyo wananchi tayari wamejenga, lakini na sisi Serikali Kuu tutafanya tathmini kuona kiasi cha fedha ambacho kitapatikana kwa ajili ya kuchangia nguvu za wananchi kukamilisha vituo hivi.

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, vituo hivi vitaendelea kukamilishwa kwa awamu. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutashirikiana kwa karibu, ahsante. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza namshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto ina Shule za Msingi 163 na Shule za Sekondari 53. Jumla ni shule 216 na watumishi ambao wapo pale kwenye shule ya msingi na sekondari mwaka 2006 ambao ni asilimia kama 40. Kuna upungufu watumishi 1,958: -

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka kupeleka walimu 1,958 kada ya uwalimu katika Wilaya ya Lushoto ili kuendeleza taaluma ya Wana-Lushoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Halmashauri ya Lushoto ina Hospitali ya Wilaya moja na vituo vya afya na zahanati 68, lakini watumishi walioko pale ni 335. Kwa hiyo, kuna upungufu wa watumishi 763. Hiyo ni idadi kubwa sana. Kwa hiyo, ni asilimia kama 35: -

Je, Serikali ina mpango gani wa dharura kupeleka watumishi wa kada ya afya 763 katika Halmashauri ya Lushoto ili kunusuru kuokoa maisha ya wananchi wa Lushoto hasa akina mama wajawazito, watoto na wazee? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya watumishi wa Sekta ya Afya na Sekta ya Elimu iko nchini kote na Serikali imechukua hatua. Kwanza hatua ya kufanya tathmini ya upungufu wa watumishi katika sekta zote, lakini pili katika mwaka wa fedha uliopita zaidi ya watumishi 9,000 waliajiriwa, lakini pia kupelekwa katika halmashauri hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi kubwa ambayo imefanyika, tumefanya tathmini kwa kuweka mpangilio na kutambua mikoa na halmashauri zenye upungufu mkubwa zaidi ikilinganishwa na mikoa na halmashauri nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna halmashauri ambazo ndani ya mkoa husika zina upungufu mkubwa ikilinganishwa na halmashauri ndani ya mkoa huo huo. Tumetoa maelekezo Makatibu Tawala wa Mikoa kufanya internal redistribution ya watumishi ndani ya mkoa ili halmashauri yenye upungufu mkubwa ndani ya mkoa ipate watumishi kwanza ndani ya mkoa. Pili, tunakwenda kwenye ngazi ya mkoa kwa maana katika nchi nzima kuhakikisha ile mikoa yenye upungufu mkubwa zaidi inapata kipaumbele kwenye ajira zinazofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Shekilindi kwamba kwenye ajira zinazofuata halmashauri yake itatoa kipaumbele cha hali ya juu kwa sababu ya upungufu huo ili kuhakikisha Walimu na watumishi wa sekta ya afya wanapata huduma bora. Ahsante sana.
MHE. EMMANUEL L. SHANGAI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ni moja ya halmashauri ambazo watumishi wanahama sana na kwa mwaka jana tu watumishi zaidi ya 93 wamehama. Pia watumishi waliohamia ni 14 tu. Kwenye ajira iliyofanyika mwezi Juni, 2021, watumishi 11 ambao waliajiriwa wakiwa na ajira nyingine baadaye Serikali iliwarudisha, lakini hakuna watumishi wengine walioletwa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wengine ambao wanataka kuhamia Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro hawapewi nafasi ya kuhamia kutoka kwenye halmashauri zao. Je, watumishi watapelekwa lini kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ngorongoro ili waweze kuhudumia wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Ngorongoro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, watumishi wanaopangiwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa wanapangiwa kulingana na taratibu na miongozo na kanuni za utumishi wa umma, lakini wanawajibika kufanya kazi katika maeneo yale isipokuwa wakiwa na sababu za msingi sana za kuomba uhamisho na sababu hizo mara nyingi ni zile za kiafya na baadhi ya sababu ambazo zinakubalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeweka mkakati wa kuhakikisha kwamba watumishi wengi ambao wanapangiwa hasa maeneo ya vijijini hawahamishwi na hivi sasa uhamisho kutoka ngazi ya Halmashauri vijijini kwenda kwenye Manispaa na Majiji umesitishwa ili kuhakikisha kwamba watumishi wengi walioko katika maeneo hayo wanaendelea kubaki pale ili kutoa huduma kwa wananchi. Hii itatuwezesha kuondokana na wimbi la watumishi kuhama kutoka halmashauri za vijijini kwenda mijini kama ilivyo Ngorongoro. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba suala hilo lilishafanyiwa kazi na Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, mkakati ni kwamba Halmashauri ya Ngorongoro ni moja ya halmashauri zenye upungufu wa watumishi na itapewa kipaumbele mara ajira zitakapopatikana ili kuweza kupunguza pengo la upungufu wa watumishi katika halmashauri hiyo. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kumekuwa na changamoto ya watu wenye bima wanapokwenda kwenye kituo cha afya ama zahanati kukosa dawa. Sasa Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inaziunganisha bima zao za afya na maduka ya private ama maduka yaliyomo ndani ya hospitali za Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tumekuwa na changamoto pia ya upatikanaji wa dawa kwa wakati na Halmashauri ya Msalala tulitenga milioni 30 kununua dawa na tulipoomba dawa kutoka MSD waliweza ku-supply dawa kiasi cha shilingi milioni 17 tu na wakakosa dawa na fedha zipo. Kwa maelezo ya Wizara ni kwamba, wanapokosa dawa kuna yule mshitiri ambaye amechaguliwa kwa ajili ya ku- supply dawa. Washitiri hawa wana-supply mkoa mzima na mikoa mingi; sasa Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba inaanzisha washitiri hawa, hawa watu wanao- supply dawa kwenye kila wilaya ili kuondoa gharama kwanza za usafirishaji wa dawa, lakini pia kupatikana kwa dawa kwa wakati? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Jimbo la Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya baadhi ya wateja wa bima kukosa dawa kwenye baadhi ya vituo vyetu ni kweli imekuwepo, lakini kwa taarifa ambazo tumeendelea kuzifanyia kazi, kasi ya ukosefu wa dawa kwenye vituo vyetu imeendelea kupungua. Hata hivyo, maelekezo ya Serikali yaliyotolewa ni kwamba, lazima vituo vyetu vyote na hospitali zetu zote na zahanati ziwe na dawa za kutosha kwa angalau asilimia 95 ya dawa zote muhimu. Hivyo, wateja hao wa bima wataendelea kuboreshewa upatikanaji wa dawa katika vituo vyetu ili kuepusha na changamoto ya kukosa dawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wazo la kuwaunganisha na maduka ya binafsi; Serikali yenyewe tumeweka mkakati kwamba hatuna sababu ya kuweka kigezo cha kuongeza maduka binafsi wakati vituo vyetu vina uwezo na vinalazimika kuweza kuwa na dawa za kutosha. Kwa hiyo njia sahihi sisi ni kuimarisha upatikanaji wa dawa kwenye vituo vyetu badala ya kupeleka kwa maduka binafsi kwa sababu kwa kuimarisha dawa hizo katika vituo, hata wale ambao hawana bima pia watanufaika na utaratibu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili kuhusiana na changamoto za upatikanaji wa dawa za wakati na hasa kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD); ni kweli kumekuwa na changamoto hiyo na Mheshimiwa Waziri Mkuu ametoa maelekezo wiki iliyopita kwamba MSD lazima wajipange kuhakikisha dawa zote zinapatikana kwa wakati na kuhakikisha kwamba vituo vyetu vinapata dawa kupitia MSD. Kwa hiyo suala hilo tunalifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mshitiri, ni kweli tulikuwa na mshitiri mmoja katika mkoa, lakini tulishatoa maelekezo kwenye mikoa yote kuongeza idadi ya washitiri, kuwa na angalau washitiri wawili, lakini hatua ya kwenda washitiri ngazi ya halmashauri bado tunaona haitakuwa na tija sana. tukishakuwa na washitiri ngazi ya mkoa ambao wana-supply vizuri, uzoefu unatuonesha tutakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Jimbo la Njombe Mjini tuna vituo viwili vya afya ambavyo vimejengwa kwa nguvu za wananchi na mapato ya ndani. Vituo hivi vimetembelewa na Mawaziri karibu wote wa TAMISEMI. Nipende kuuliza; ni lini sasa vituo hivi ambavyo viko tayari kwa asilimia 100 vitapata vifaa na watumishi ili viweze kuanza kutoa huduma kwa wananchi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mwanyika kwa kuwasemea kwa ufasaha sana wananchi wa Jimbo la Njombe Mjini na kwa kweli hoja hii ameizungumza hapa zaidi ya mara mbili na sisi kama Serikali tumhakikishie tulishachukua hoja hii kwa ajili ya kupeleka vifaatiba kwenye vituo vile viwili vya afya, lakini pia kufanya mpango wa kupata watumishi pale na fedha tayari ziko MSD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosubiri ni manunuzi ya vifaatiba hivyo ili viweze kupelekwa kwenye Jimbo la Njombe Mjini. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili linafanyiwa kazi. Ahsante.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. napenda kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa sasa Serikali inasema inatumia mfumo wa online katika kupokea maombi ya Walimu; na kwa kuwa malalamiko ni mengi ambayo yalikuwa yanahusu Walimu kutoajiriwa kutokana na mwaka waliohitimu. Sasa napenda kuiuliza Serikali; haioni sasa kuna haja pale nafasi zinapopatikana za kuajiri waweke ukomo kwa wale wanaoomba kwamba mwaka huu tutapokea maombi ya wahitimu wa vyuo vya Walimu wa mwaka fulani hadi mwaka fulani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Walimu kutoajiriwa muda mrefu kunawafanya wakae mitaani, lakini pia miaka inapita wengine wanaweza kutoajiriwa kwa sababu ya umri walionao. Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuwapatia refresher courses kwa sababu wale Walimu waliokaa muda mrefu wanapokuwa hawakuajiriwa wanasahau baadhi ya mafunzo yao na hata zile methodologies za kufundisha. Je, Serikali haioni kwamba wanastahili kupewa refresher courses na wako tayari kuzitoa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mfumo huu wa Online Teachers’ Employment System ni mfumo ambao kwanza umeleta uwazi, lakini pia umeleta haki kwa wale Walimu wenye sifa kuajiriwa bila kuwa na upendeleo wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuwa na ukomo wa ajira, tumesema vigezo vyetu vilikuwa vitatu; kigezo cha kwanza kilikuwa ni wale waliohitimu muda mrefu zaidi. Ndiyo maana zaidi ya asilimia 75 ni wale waliohitimu mwaka 2014 hadi 2017. Hiyo consideration iliwekwa ili wale wenye umri mkubwa wapate nafasi ya kuajiriwa kabla ya umri wao wa miaka 45 kufikiwa na kukosa fursa ya kuajiriwa Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, wale walioajiriwa mwaka 2018 hadi 2019, wahitimu wa miaka hiyo walikuwa wana mahitaji maalum na walio wengi walikuwa wenye ulemavu. Kwa hiyo bado itakuwa siyo sahihi sana kuweka kigezo cha kwamba tuajiri miaka miwili au mitatu; kwanza hatujui ni Walimu wangapi watajitokeza katika miaka hiyo kulingana na mahitaji yetu na ni wangapi watachujwa na kuwa na sifa husika. Tunaweza tukasema kati ya 2018 na 2019 lakini wakatokea wachache wenye sifa na tukakuta tumeweza kuathiri zoezi hilo. Kwa hiyo tutaendelea kuhakikisha kwamba tunawapa fursa wote kuajiriwa, lakini tunatumia vigezo vyetu kuona nani kwa sasa apate ajira na nani anaweza akapata ajira awamu inayofuata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Walimu kukaa muda mrefu zaidi bila ajira, ni kwa sababu tumekuwa na baraka nzuri kwamba Walimu wengi wanazalishwa kwenye vyuo vyetu kila mwaka ikilinganishwa na kasi ya ajira ambayo ipo Serikalini lakini pia kwenye taasisi binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la msingi ni kwamba mara baada ya kuajiriwa katika shule zetu kuna taratibu za refresher courses na on-job training na mentorship ambazo watazipata. Kwa hiyo automatically ukishaingia kwenye shughuli zao za kazi watapata mafunzo kazini na kuwawezesha kuwa competent zaidi. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Serikali ya Chama Cha Mapinduzi inafanya kazi nzuri sana ya kujenga majengo ya sekondari kwenye shule nyingi sana hapa nchini. Katika Jimbo langu la Bunda kuna shule nane, zina upungufu wa Walimu wa sayansi 56, na tunaposema walimu wa sayansi maana yake tuna masomo ya baiolojia, fizikia, kemia na hisabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu, je, ni lini Walimu 56 wa sayansi watapelekwa katika Shule za Sekondari za Hunyari, Chamuriho, Mihingo, Mekomariro, Salama, Esparento, Makongoro, Nyamang’uta; ni lini hawa Walimu 56 watakwenda huko? Tunapouliza maswali haya maana yake ni kwamba watoto wako darasani, lakini Walimu wa sayansi hawapo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa Walimu wa sayansi bado ni changamoto ambayo Serikali tunaitambua na tumeweka mkakati wa kuhakikisha katika ajira zetu tunaweka kwanza kipaumbele cha Walimu wa masomo ya sayansi. Katika zile ajira ambazo zimepita asilimia kubwa ya walimu walioajiriwa ni Walimu wa masomo ya sayansi. Hata hivyo, tumeweka mkakati pia kwenye ajira zinazofuata, walimu ambao wataajiriwa kwa kiasi kikubwa ni Walimu wa sayansi ili kuwezesha kupunguza pengo la upungufu wa Walimu wa sayansi katika shule zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Getere kwamba wakati wa ajira hizo Halmashauri yake ya Bunda na shule hizi alizozitaja zitapewa kipaumbele kupata Walimu hawa wa sayansi ili kupunguza pengo la Walimu 56 ambao hawapo katika halmashauri hiyo. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini naomba niongeze maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa Serikali imefanya jitihada kuweza kuleta Walimu, lakini utaona kwamba, asilimia 71 ni kubwa sana kwa jimbo letu la Temeke au Wilaya nzima ya Temeke. Sasa je, Serikali haioni kwamba, inaweza kufanya jitihada za ziada ili kuweza kupata vibali kwa halmashauri zetu kuweza kuajiri Walimu kwa mikataba, hao wa sayansi ili tuone kwamba, elimu sasa inaendelea mpaka hapo Wizara itakapokuwa imepata namna ya kuweza kuajiri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kuhusiana na vifaa katika sekondari zetu, je, bado haionekani ya kwamba, tunaweza tukapata vibali hivyo tukaweza kununua vifaa hivi kwa ajili ya maabara zetu, badala ya kusubiria wadau na sisi tuna fedha katika manispaa zetu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali imeendelea kufanya jitihada za makusudi, ili kupunguza pengo la upungufu wa Walimu wa sayansi katika shule zetu za sekondari, lakini mikataba ya ajira kwa watumishi wa umma; tayari Serikali ilishaandaa modal ya mikataba kwa halmashauri zetu kuajiri watumishi kwa mkataba kwa kutumia mapato ya ndani ya halmashauri.

Kwa hiyo, kibali kilishatolewa na watumishi wote wa sekta ya afya, sekta ya elimu na wengine ambao halmashauri kwa uwezo wa mapato ya ndani wana uwezo wa kuwalipa mishahara kwa mikataba, kibali kilishatolewa na tunatia shime kwamba, waendelee kutumia fedha za mapato ya ndani kuajiri watumishi kwa ajili ya kupunguza pengo la upungufu wa watumishi hao.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na vifaa vya sayansi kwa shule za sekondari, nalo linafanana na jibu langu la kwanza kwamba, mapato ya ndani ni sehemu ya fedha za Serikali kwa hiyo, kazi yake ni pamoja na kutatua changamoto zikiwemo za upungufu wa vifaa vya sayansi katika shule zetu. Kwa hiyo, lazima halmashauri zitenge fedha hizo ili kupunguza mapengo ya vifaa hivyo. Nakushukuru.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke ina upungufu wa Walimu 6,300. Je, Serikali haioni haja ya kuleta Walimu wapya kujaza nafasi zote za Walimu waliofariki na kustaafu wa Manispaa ya Temeke?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Chaurembo Abdallah, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, watumishi wetu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa na maeneo mengine ya Serikali, wale ambao kwa sababu moja ama nyingine wanastaafu ama kufariki dunia, utaratibu wa kujaza nafasi zao unafuata utaratibu wa ajira za kawaida, lakini kwa kuzingatia uhitaji katika halmashauri husika.

Kwa hiyo, wale watumishi ambao katika Halmashauri ya Temeke wamestaafu, wanafahamika idadi yao, lakini waliofariki idadi yao inafahamika na wakati wa vibali vya ajira moja ya maeneo ambayo yanawekewa kipaumbele ni kujaza nafasi hizo. Nakushukuru.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo inaendelea kupambana kuwasaidia wananchi ili waweze kujikwamua kiuchumi: -

Mheshimiwa Spika, soko hili la ujirani mwema ni soko kati ya nchi ya Tanzania na Burundi. Kama nilivyouliza kwenye swali langu la msingi, mahali pale Serikali imeweka pesa kujenga yale mabanda kwa ajili ya biashara, lakini hakuna kituo cha polisi, hakuna TRA, wala hakuna uhamiaji, hivyo, kufanya utendaji wa soko lile kuwa hafifu kwa sababu ya hatarishi hii.

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa mpaka uko kilometa tano ndani ya nchi ya Tanzania kwa hiyo, hata pale ambapo uhamiaji wanafanya shughuli zao za kawaida inasababisha usumbufu sana kwa wananchi. Hivyo, napenda kujua ni lini Serikali itaweka vile vipaumbele vya One Stop Centre kama nilivyouliza kwenye swali langu la msingi, ikiwamo forodha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Muhambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Dkt. Florence kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuwasemea wananchi wa Muhambwe, lakini nimhakikishie kwamba, hoja hizi zote ambazo amezileta Serikali imeanza kufanyia kazi, likiwemo suala hili la kupima maeneo ya viwanja 145 kuzunguka soko, ili tuweze kupata maeneo kwa ajili ya kujenga Vituo vya Polisi, Forodha, lakini pia nae neo la Uhamiaji. Kwa hiyo, mara baada ya ramani zile kukamilishwa ambazo tayari mchakato unatarajiwa kuanza wakati wowote, sasa tutaenda kuomba kwenye sekta husika waweze kujenga vituo hivi na kuwezesha soko kufanya kazi vizuri. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, Mji wa Bukoba uko katika mkoa unaopakana na nchi jirani zaidi ya tatu. Je, ni lini Serikali itajenga soko kuu Bukoba Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mji wa Bukoba ni miongoni mwa miji ambayo iko kwenye mpango mkakati ambao utakwenda kujenga masoko, barabara, vituo vya mabasi vya kisasa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Oliver Semuguruka, lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Stephen Byabato, Mbunge wa Jimbo la Bukoba Mjini, amekuwa mfuatiliaji wa mara kwa mara na Serikali iko kwenye hatua za mwisho za kuanza utekelezaji wa mradi huo. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba, soko hilo, lakini pamoja na maeneo hayo mengine yatafayiwa kazi baada ya mradi huo kuanza. Nakushukuru sana.
MHE. NICODEMUS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, Ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini namwomba Waziri apate muda twende tukafanye ziara kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe. Mbogwe ni mji ambao umezingirwa na mapori mengi, hivyo wananchi wa pale wanapata tabu sana jinsi ya kuishi na mapori katikati japokuwa mapori yale hayana sifa ya kuwa na hifadhi. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri siku moja twende tuongozane naye ili kusudi twende tukashauriane vizuri ili wananchi wale waweze kuishi katika hifadhi zile. Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimepokea ombi hilo na baada ya kikao hiki tutapanga baada ya Bunge tuweke ratiba ya kwenda Mbogwe. Nashukuru sana.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Matatizo yaliyoko kwenye Pori la Mbogwe ni sawa kabisa na matatizo yaliyoko kwenye Jimbo la Geita Vijijini, Hifadhi ya Rwande, ambayo kimsingi ilishapoteza sifa ya hifadhi.

Sasa ombi langu Mheshimiwa Waziri, atakuwa tayari baada ya vikao hivi kutembelea Jimbo la Geita Vijijini ili aweze kuja kuona lile pori badaye tuwe na utaratibu wa kuwarudishia wananchi waweze kuendelea kulima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Musukuma kwenda jimboni kwake na kutembelea pori hilo ili pamoja na Wizara ya Ardhi na wadau wengine tukubaliane namna ya kuli-manage ili wananchi waweze kupata fursa nzuri. Nashukuru sana.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali moja la nyongeza. Chuo hiki cha Bandari ni chuo ambacho kiko kwenye ukanda huu wa Afrika Mashariki, na ni chuo muhimu sana kwa ajili ya mafunzo haya; na kwa sababu vijana wanaokwenda kufundishwa pale wanahitaji kufundishwa kwa vitendo; na kwa sababu chuo hiki kina tatizo la kuwa na meli ya mazoezi. Je, ni lini Serikali sasa itatenga fedha kwa ajili ya kununua meli ya mazoezi kwa ajili ya kuwasaidia vijana kwa ajili ya mafunzo ya vitendo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ameuliza ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mafunzo. Nimhakikishie tu Mheshimiwa kwamba, katika suala hili, pamoja na mambo mengine ya uboreshaji wa chuo hicho, ikiwa ni sambamba na ujenzi unaoendelea, zipo pia fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya vifaa vya kufundishia na kwenye hili suala la meli ni sehemu ya mpango huo. Kwa hiyo kulingana na upatikanaji wa fedha tutalikamilisha hilo na Serikali hii imekuwa ikifanya kazi kwa speed, tutalikamilisha. Ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza naomba nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa stendi hii ulikuwa ni sehemu ya ujenzi wa barabara miaka sita iliyopita, ambapo ilikuwa ni sehemu ya fedha za mkopo ya World Bank na baada ya muda uli-phase out na fedha hizi zikabaki kwenye Mfuko wa Serikali. Sasa swali langu namba moja; kwa kuwa mkopo huu ulikuwa wa pamoja, fedha zilizobaki kwenye utekelezaji wa mradi huu wa awali zilienda wapi?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, nashukuru kwa ujio wa mradi wa pili wa World Bank ambao ni TACTIC ambao unatarajia kuanza hivi karibuni. Sasa kilichosababisha stendi isijengwe awamu ya kwanza ni kwa sababu utangazaji wa miradi unakwenda kwa awamu. Wanatangaza barabara moja baada ya nyingine na mradi mwingine baada ya mwingine na matokeo yake mradi una-phase out na fedha zinaisha. Je, kwa nini Wizara isiwashauri wafadhili, miradi hii ikatangazwa kwa pamoja ili iweze kutekelezwa kwa pamoja kuepuka tatizo lililotokea hapo awali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyingeza ya Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Kanyasu kwa kuwasemea kwa dhati kabisa wananchi wa Geita Mjini. Pili, nimhakikishie kwamba mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa, pamoja na kwamba ulisanifiwa na kupangwa kufanyika pamoja miaka sita iliyopita, changamoto iliyojitokeza ilikuwa ni upungufu wa fedha katika kutelekeza mradi wa stendi hiyo. Stendi hiyo ni ya kisasa, ni kubwa na inahitaji fedha nyingi na ndiyo maana kwenye awamu ile ya kwanza haukuweza kukamilika.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba kwenye mwaka wa fedha 2022/2023, tayari usanifu umefanyika na uko hatua za mwisho na utatekelezwa kupitia mradi wa TACTIC ambapo tutajenga barabara za lami kilometa 15 pamoja na stendi hii ya kisasa katika Mji wa Geita. Ahsante sana.
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwa kuwa hitaji la stendi lililoko Jimbo la Geita Mjini ni sawa kabisa na lile lililoko katika Jimbo la Mwanga; na kwa kuwa mwezi Novemba mwaka jana Mheshimiwa Rais alipotembelea Mkoa wa Kilimanjaro aliwaahidi wananchi wa Mwanga stendi ya kisasa pale Mwanga.

Swali langu je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hii ya Mheshimiwa Rais kwa wananchi wake wa Mwanga? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Tadayo, Mbunge wa Mwanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ahadi ya Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan tayari tumeshaipokea Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tumeshaifanyia tathmini na tunatafuta fedha wakati wowote ahadi hiyo itatekelezwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari kazi imeanza kwa ajili ya kujenga stendi ya kisasa pale Mwanga. Ahsante. (Makofi)
MHE. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii.

Kwa kuwa hitaji hili la stendi katika Mji wa Geita ni sawasawa na kilio cha muda mrefu cha wananchi wa Biharamulo cha kupata stendi ya kisasa pale, ni lini sasa Serikali itaanza ujenzi wa stendi ya kisasa katika Mji wa Biharamulo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa miundombinu ya stendi za kisasa, ujenzi wa barabara pamoja na ujenzi wa masoko vyote ni vipaumbele katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Kazi ambayo Serikali tumeelekeza, kwanza halmashauri zifanye tathmini ya uwezo wa mapato yao ya ndani na kuweka kipaumbele cha kuanza ujenzi wa miundombinu hiyo, zikiwemo stendi za kisasa kwa kutumia mapato ya ndani kwa zile halmashauri zenye uwezo wa mapato ya ndani. Zile halmashauri ambazo hazina uwezo wa mapato ya ndani waandae maandiko ya miradi ya kimkakati ya stendi hizo na kuyawasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Wizara na Mipango ili tufanye tathmini na kutafuta fedha za kuwezesha kujenga stendi za kisasa za kimikakati katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Ezra Chiwelesa kwamba, wafanye tathmini Biharamulo waone uwezo wao wa mapato ya ndani, lakini kama hautoshi walete mradi wa kimkakati ili fedha itafutwe kwa ajili ya kujenga stendi ya kisasa pale Biharamulo. Ahsante. (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri; kwa kuwa katika eneo la TaCRI pale Mbimba Vwawa lilitengwa kwa ajili ya kujenga stendi kubwa ya Mkoa wa Songwe. Je, ni lini stendi hiyo itaanza kujengwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba baada ya stendi ya mkoa kukosekana katika Mkoa wa Songwe ulifanyika mpango wa kuandaa eneo kwa ajili ya ujenzi wa Stendi ya kisasa ya Mabasi ya Mkoa wa Songwe katika eneo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelitaja. Nimhakikishie kwamba lengo la Serikali bado liko vile vile na mipango inafanyika ya tathmini ya mahitaji ya fedha na kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga stendi ile. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mpango bado upo na taratibu za kutafuta fedha zinaendelea ili tuanze ujenzi. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa sababu mazingira ya ukamilishaji wa vituo hivi umechangiwa kwa namna moja au nyingine kuonekana kwamba kuna maeneo ambayo bado hayajakamilika, kwa mfano Nagaga, Mnavira pamoja na Chiungutwa kuna fedha ambazo hazijatimia pale, kwa sababu bajeti nzima ilikuwa shilingi milioni 500 lakini wamepewa shilingi milioni 400 na hivyo kusababisha baadhi ya majengo kama vile wodi ya akinamama pamoja na majengo ya ultrasound kutokamilika.

Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha majengo haya yaliyokosekana? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa vituo vya afya nchini kote unakwenda kwa awamu. Tunapeleka fedha awamu ya kwanza, tunajenga majengo ya kipaumbele ili kuwezesha vituo kuanza kutoa huduma za msingi, lakini tunatafuta fedha kwa ajili ya awamu ya pili ili kukamilisha majengo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo fedha ambazo zilipelekwa Nagaga na Mnavira zilikamilisha sehemu ya kwanza ya majengo, lakini milioni 100 ambayo inabaki itapelekwa ili kukamilisha wodi ya wanawake pamoja na jengo hilo la ultrasound. Ahsante sana.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, kwa kutuwezesha fedha hizo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa mapenzi yake mema, lakini naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Lindi Mjini tuna kata 20 lakini kata 13 ziko katikati ya Mji, lakini ukiangalia wananchi wale, katika kata 13 zaidi ya watu 70,000 wanakosa mahali pa kukimbilia kwa maana ya kituo cha afya. Sasa ninaomba kuiuliza Serikali watatusaidiaje kuhakikisha kwamba tunapata Kituo cha Afya Lindi Mjini kuwasaidia wakazi wa kata 13 waishio Lindi Mjini?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili katika Kata ya Kitumbikwela upande wa pili wa bahari pana kituo cha afya lakini bado hakijakamilika, wanawake wanapata changamoto wakati wa kujifungua na wanapolazimika kufanyiwa upasuaji, kivuko wakati mwingine kinakuwa kina changamoto.

Kwa hiyo, ninaomba kuiuliza Serikali ni lini wataweza kutusaidia kuboresha Kituo cha Afya cha Kitumbikwela ili wanawake wajawazito waweze kuhudumiwa pale? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Jimbo la Lindi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Hamida Mohamed kwa kuwasemea kwa dhati kabisa wananchi wa Lindi Mjini na mimi nimhakikishie kwamba Serikali hii sikivu ya Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan tutaendelea kushirikiana naye na kuhakikisha kwamba wananchi wa Lindi wanapata maendeleo ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na vituo vya afya katika Jimbo la Lindi Mjini; ni kweli kwamba wana vituo vya afya vichache. Lakini Serikali tumeshatoa fedha kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Mnazimmoja, lakini tumepeleka fedha kwa ajili ya kujenga Hospitali kubwa ya kisasa ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini bado tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuendelea kujenga vituo vya afya katika kata za kimkakati ambazo hazina vituo vya afya.

Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba Serikali inafahamu changamoto hiyo na mipango inaandaliwa kuhakikisha Manispaa ya Lindi tunapata vituo vya afya.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Kitumbikwela ni kweli Kata ya Kitumbikwela ipo upande wa pili wa bahari na njia kuu ya kuvuka pale ni kwa kutumia mapantoni lakini pia na boti. Kwa hiyo, kwa kweli tunahitaji kuboresha kituo kile cha afya ndio maana tulianza ujenzi kwa awamu ya kwanza, sasa tutakwenda kujenga miundombinu iliyobakia zikiwemo wodi na majengo mengine kwa awamu ya pili ili kuhakikisha huduma zinakwenda vizuri. Ahsante. (Makofi)
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante; kwa kuwa Serikali inajenga Hospitali za Wilaya na Vituo vya Afya nchi nzima na kwa kuwa baadhi ya hospitali za Wilaya ni kongwe.

Je, Serikali haioni haja ya kutenga fedha kwa ajili ya ukarabati hospitali za wilaya ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Pangani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantumu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na Hospitali za Halmashauri kongwe ambazo zilijengwa miaka mingi. Zipo ambazo zimejengwa baada ya uhuru mapema, lakini zipo ambazo, zilijengwa hata kabla ya uhuru na kwa kweli miundombinu yake sasa ni chakavu. Lakini pia haziendani na kiwango cha hospitali za halmashauri ambazo sasa tunazihitaji. Kwa kutambua hilo Serikali tumefanya tathmini ya hospitali zote za Halmashauri kongwe na tumekwisha ziainisha. Tunaweka mpango, baada ya kukamilisha hospitali za Halmashauri 28, sasa tutakwenda kukarabati na kupanua hospitali zile kongwe ikiwepo Hospitali hii ya Pangani. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na upungufu mkubwa wa walimu wa sayansi katika Mkoa wa Lindi na hii inaleta ufaulu hafifu kwa wanafunzi katika masomo hayo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupatikana walimu wa sayansi kwa haraka iwezekanavyo kunusuru shida hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia naona kwenye majibu kuna upatikanaji/kibali cha kuajiri walimu 10,000. Katika hilo naomba sana Serikali watupe kipaumbele Mkoa wa Lindi, kwa sababu tuna changamoto kubwa ya walimu. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tecla Mohamedi Ungele Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumekuwa na upungufu wa walimu wa sayansi katika shule zetu za sekondari nchini kote na tumefanya tathmini, kubaini mahitaji ya walimu wa sayansi angalau kuwezesha shule zetu kuwa na walimu wanaoweza kutosheleza mahitaji ya wanafunzi. Ndio maana katika ajira zilizopita asilimia 75.5 ya walimu wote walioajiriwa walikuwa ni walimu, wa masomo ya sayansi na utaratibu wa kuendelea kutoa kipaumbele kwa walimu wa sayansi katika ajira zinazofuata utaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la kibali cha walimu katika halmashauri hiyo kupewa kipaumbele katika walimu 10,000, tutawapa kipaumbele na kazi iliyofanyika tumeainisha Mikoa yote yenye upungufu mkubwa zaidi wa walimu na watumishi wengine. Mikoa hiyo na Halmashauri hizo zitapewa kipaumbele wakati wa kuajiri watumishi hao. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru; Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ina upungufu wa watumishi zaidi ya 1,700 wa kada ya ualimu. Kwa sababu za kijiografia watumishi wengi wamekuwa wakipangiwa wanaripoti baadaye wanaondoka.

Sasa Serikali haioni sababu za msingi na kwa sababu maalum kutoa kipaumbele kwa watu wenye taaluma ya ualimu, wazawa wa Ukerewe wakaajiriwa na wakapangiwa eneo la Ukerewe kuweza kuwasaidia watu wa jamii ile? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na changamoto ya baadhi ya watumishi hasa wanaoajiriwa katika maeneo ya Halmashauri za vijijini kuomba uhamisho mapema mara baada ya kuajiriwa. Lakini mambo mawili yamefanyika Serikalini; la kwanza, katika ajira zilizopita tulihakikisha kila anayeomba ajira anaomba ajira kwa maana ya shule husika na Halmashauri husika. Tulikubaliana katika mikataba kwamba lazima wakae angalau miaka mitatu katika vituo vyao vile ambavyo wameajiriwa.

Kwa hiyo, suala hilo litakuwa endelevu tutahakikisha kwamba mtumishi yeyote anayeajiriwa, akishaajiriwa katika Halmashauri na shule hiyo lazima akae angalau miaka mitatu ili kuepusha wimbi la kuhama kwa maeneo ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala la kuwa na watumishi wazawa ni jambo jema na tumeendelea pia kuwapa kipaumbele. Lakini pia tunapenda utaifa kwa maana ya kwamba, waalimu wanaotoka Ukerewe waende maeneo mengine, lakini wanaotoka maeneo mengine waende pia Ukerewe ili kujenga utaifa wa nchi yetu, badala ya kuwa na watu wa aina moja katika eneo lile. Lakini tutaendelea kuhakikisha kwamba waalimu wanaopangiwa maeneo hayo, wanabaki na pia tunaendelea kudhibiti sana uhamisho katika maeneo hayo, ahsante. (Makofi)
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; pamekuwa na wimbi la vijana wengi waliomaliza vyuo vya elimu, kujitolea kwenye shule zetu za TAMISEMI.

Je, Serikali imejipanga vipi ku-accommodate vijana hao katika kibali cha ajira kilichotoka cha kuajiri vijana 10,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na walimu wanaojitolea katika shule zetu za Serikali, lakini pia na watumishi wa kada nyingine wakiwemo watumishi wataalam wa afya. Utaratibu ambao umewekwa na Serikali ni kuhakikisha wakati tunakwenda kutoa ajira kupitia vibali vya Serikali, wale waalimu ambao wanatambulika rasmi wanajitolea katika shule zile wanapewa kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndio maana kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba tunakwenda kuweka utaratibu wa kutumia mfumo wa kielektroniki, ambao utawatambua rasmi walimu na watumishi wengine wanaojitolea ili wapewe kipaumbele kwenye ajira zinazofuata. Kwa hiyo, hili tumelichukua tunaendelea kulifanyia kazi ili kuweza kurahisisha utendaji wake. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Vicent Paul Mbogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali, lakini nina jambo moja ambalo nataka nimwambie Naibu Waziri; kwamba pesa hizo shilingi milioni 25 zilizotengwa kwa ajili ya ku-repair hizo boti na magari ni kidogo. Kwa sababu hizo boti mbili ziko beyond repair na zimekuwa grounded kwa miaka mitatu. Nataka kujua, Serikali inawaambia nini wananchi wa Jimbo la Nkasi kusini; kwamba itawapelekea lini boti mpya ili waachane na huu mpango wa kutenga shilingi milioni 25 ambazo hazitoshelezi kurekebisha hizo boti? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sangu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa matengenezo ya magari na vifaa mbalimbali katika Halmashauri kwanza ni jukumu la Halmashauri kutenga kwenye bajeti zao; kufanya preventive maintenance ya vifaa pamoja na magari. Ikiwa Halmashauri haina uwezo wa kutosha wa kifedha wa wa kufanya matengenezo makubwa kama hizi boti ambazo ziko beyond repair, wanatakiwa kwanza kufanya tathmini ni kiasi gani cha fedha kinatakiwa kufanya matengenezo yale; na pili, kuomba maombi maalum ya kupata vifaa hivyo kwa ajili ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kwanza wafanye tathmini, hizo boti zinahitaji kiasi gani kufanya matengenezo? Pili, Halmashauri katika vyanzo vyao wana uwezo wa kiasi gani? Kisha wasilishwe sehemu ile inayobaki ili Serikali iweze kuona namna ya kuongeza nguvu kwa ajili ya matengenezo hayo. Ahsante.
MHE. JANEJELLY J. NTATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali; na niwapongeze kwa kutenga hizo fedha na kuzipeleka kwa ajili ya kufanya malipo; lakini nina maswali mawili (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuna watumishi ambao wamestaafu lakini walihusika kwenye zoezi hili, wengine wamepewa nafasi za uteuzi na walihusika kwenye zoezi hili: Je, Serikali mmejipangaje kuhakikisha hizi fedha zinafika kwa walengwa? (Makofi)

(b) Kwa kuwa ulipaji wa malipo ya Watumishi wa Afya ni endelevu, Serikali mmejipangaje kuwa mnawalipa kwa wakati? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Janejelly James Ntate, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, nipokee pongezi zake nyingi kwa Serikali ambapo baada ya watumishi wale kufanya kazi hiyo, imehakikisha imepeleka shilingi bilioni tatu kwa ajili ya watumishi kupata haki zao. Pili, watumishi waliostaafu au watumishi waliopata teuzi mbalimbali ambao kwa wakati huu hawapo kwenye Halmashauri, bado taarifa zao zote za kiutumishi na haki zao zipo katika Halmashauri husika na baada ya kuchakata malipo hayo, watapata haki zao kwa sababu taarifa zote zipo kwenye Halmashauri. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taarifa zao zote zipo na malipo watayapata pale walipo kwa kadri wanavyostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na utaratibu wa malipo kwa watumishi wa huduma za afya, ni zoezi endelevu na Serikali imeendelea kuboresha utaratibu wa kuhakikisha watumishi wanaofanya kazi masaa ya zianda wanalipwa kwa wakati. Kwa kweli hali kwa sasa inaendelea kuimarika na mpango huu ni endelevu, tutahakikisha kwamba tunatafuta fedha kwa wakati na kuhakikisha kwamba watumishi wale wanapata haki zao kwa wakati.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Pia naomba niipongeze Serikali kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kuanzisha mamlaka mapya ya utawala ni kusogeza huduma kwa wananchi, na suala hili limeletwa leo lina mwaka mzima uchambuzi unaendelea. Je, ni lini sasa wananchi hawa watapata jibu sahihi kwamba wilaya yao ianze mara moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniventura Destery Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuanzisha mamlaka mpya ni kweli kunasogeza huduma karibu zaidi na wananchi, lakini pia kuna gharama mbalimbali ambazo zinaendana na kuanzisha makao mapya ya halmashauri. Na ndiyo maana halmashauri nyingi ambazo zimeanzishwa na maeneo mengine ya utawala bado Serikali inawekeza fedha kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu, ujenzi wa majengo ya utawala halmashauri, ujenzi wa ofisi mbalimbali za maeneo hayo ili kuwezesha wananchi kupata huduma bora kupitia ofisi hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunakwenda kwa hatua, tuko hatua hii, tunakamilisha maeneo hayo na baadaye tutakwenda kwenye halmashauri nyingine na sisi tutashauri mamlaka kadri itakavyoona inafaa kwa ajili ya kuona uwezekano wa kuanzisha mamlaka hizi. Ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Mbulu Vijijini tumeshapata halmashauri na majengo yameshakamilika, na kwa kuwa Mbulu ina halmashauri mbili; je, lini mnatupatia mamlaka ya kuwa na wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu ina Halmashauri ya Mji na Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu Vijijini. Na halmashauri hizi zote zinaendelea kuwekewa miundombinu ya ujenzi ikiwepo Halmashauri ya Mbulu Vijijini ambako jengo la kisasa kabisa la utawala limejengwa, limekamilika na hatua hiyo itawezesha halmashauri hii kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwa halmashauri zile mbili na kwa ukubwa wa jiografia ile, tunafikiri bado tunastahili kuboresha kwanza halmashauri zilizopo na baadae kama kutakuwa na sababu ya kuanzisha halmashauri nyingine basi tathmini itafanyika na wananchi watapewa taarifa hiyo. Ahsante.
MHE. REUBEN N. KWAGILWA: Mheshimwa Naibu Spika ahsante sana, naomba niulize swali moja la nyongeza kutokana na majibu ya swali langu la msingi. Mkataba aliopewa mkandarasi ambaye yupo site sasa kuujenga mnada wa Nderema, pamoja na kwamba unajenga miundombinu ya muhimu, bado kuna miundombinu ya msingi ambayo haijaainishwa kwenye mkataba na haimo kwenye mkataba, lakini miundombinu hii ni muhimu sana kwa mnada ule. Mathalani vibanda vya kupumzikia, mahali pa kupandishia ng’ombe kwenye magari pamoja na machinjio.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haifikirii pana umuhimu sasa wa kwenda kufanya marekebisho kwenye mkataba ule ili miundombinu hii iweze kuingizwa kwenye mkataba huu wa mkandarasi aliyepo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Reuben Nhamanilo Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tumepeleka milioni 287 na mkandarasi atajenga miundombinu ikiwemo uzio, ofisi, mazizi manne, maeneo ya kushushia mifugo, lakini pia vyoo na miundombinu mengine. Hii ni hatua ya kwanza, hatua ya pili tutakwenda ku-consider miundombinu ambayo Mheshimiwa Mbunge ameisema ili tutenge bajeti kuhakikisha mnada ule unakuwa na miundombinu yote muhimu. Nakushukuru.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; ni zaidi ya miaka 10 sasa tangu Mamlaka ya Mji Mdogo wa Ilula imeanzishwa, ningependa kujua ni tathmini gani au ni utaratibu gani unatumika ili kupandisha hadhi kutoka kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo kwenda kuwa Halmashauri?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ningependa kujua katika ugawaji wa halmashauri kipo kigezo cha idadi ya watu na katika maeneo yenye hifadhi kubwa ya misitu na maeneo yaliyohifadhiwa na mbuga kama Kilolo kigezo hiki kinakuwa tishio kusababisha kuchelewa kugawa kwa halmashauri pamoja na ukubwa wake. Je Serikali iko tayari kuangalia kigezo hiki na kuangalia zaidi ukubwa ili wananchi waweze kufikiwa na huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, uanzishaji wa mamlaka mpya zikiwepo halmashauri za miji zinategemea kukidhi vigezo vilivyowekwa ili halmashauri iweze kupewa mamlaka halisi ya kuwa halmashauri kutoka malmaka ya mji mdogo. Ni kweli kwamba Mamlaka ya Mji Mdogo wa Ilula ina zaidi ya miaka 10 lakini taratibu za kuomba kuwa Halmashauri ya Mji ni zilezile ambazo zinatumika kuomba Halmashauri ya Wilaya. Kwa maana vikao vya kisheria katika vijiji na mitaa, kata ngazi ya wilaya pamoja na DCC na RCC. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na kuomba Wilaya igawiwe kuwa wilaya mbili lakini pia wafuate utaratibu huo kwa Halmashauri ya Mji wa Ilula ili tathmini ifanyike kuona kama kama inakidhi vigezo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na ukubwa wa kijografia wa Wilaya ambayo ina misitu mingi lakini wananchi wachache. Kigezo cha wananchi ni kigezo muhimu sana kwa sababu tunapeleka mamlaka mpya kuhudumia wananchi kwa hiyo idadi ya wananchi ndio sababu ya msingi zaidi ya kutenga halmashauri mpya badala ya eneo la misitu, lakini pia kwa maana ya ukubwa ambao hakuna idadi ya watu. Kwa hiyo, suala hilo ni muhimu na tutaendelea kuhakikisha kwamba, tunalizingatia katika kugawa mamlaka mpya. Ahsante.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Tatizo la kugawa maeneo ya utawala lililokuwa limetolewa na Mheshimiwa aliyemaliza, linafanana sana na tatizo lililopo katika Jimbo langu la Kigoma Mjini na hasa kugawa maeneo ya utawala ya kata. Maombi tayari yamekwishapelekwq kwa zaidi ya miaka mitatu mfululizo kwenye Wizara husika. Je, ni lini Serikali itafikiria kufanya kazi hii ya kugawa kata. Zipo kata ambazo zina wakazi wengi, zina mitaa mingi, Kata kama za Mwanga Kaskazini, Mwanga Kusini, Buzebazeba na Kibirizi huko Kigoma. Je, ni lini Serikali itachukua hatua hii ili kuwarahasishia watu huduma za kiutawala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilumbe N’genda, Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Halmashauri zimeendelea kuwasilisha maombi ya kugawa maeneo mapya ya utawala kwa maana ya kata na nikiri kwamba Serikali tumepokea zikiwepo Kata za Kigoma Mjini, tathmini zinaendelea na baada ya tathmini hizo na kuangalia mazingira hayo, tutashauri mamlaka husika kwa maana ya mamlaka inayoweza kugawa maeneo hayo ili tuweze kufikia hatua ambayo inahitajika. Kwa hivyo nimhakikishie Mbunge kwamba, suala hilo lipo linafanyiwa kazi. Nashukuru.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Naibu Spika nakushukuru. Kwa kuwa taratibu za kuigawa Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba kulipatikana Halmashauri ya Sumve ambayo ndio ina Jimbo la Sumve zimeshakamilika katika ngazi zote mpaka ngazi ya mkoa na tunasubiri tamko la ngazi ya juu kupatikana kwa Halmashauri ya Wilaya Sumve. Je, nini tamko la Wizara kuhusu upatikanaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Sumve ambayo ni tamanio kubwa la watu wa Sumve na itasaidia sana kusogeza huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasalali Mageni, Mbunge wa Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, taratibu za kugawa maeneo mapya ya utawala tayari zimepokelewa kwa halmashauri zote ambazo zimewasilisha kupitia utaratibu wa kisheria na kanuni na tathmini inaendelea. Mara baada ya kukamilisha tathmini hizo mamlaka husika itafanya maamuzi ya kugawa ama kutoa muda kwa ajili ya kuboresha maeneo ambayo yatakuwa na upungufu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo lipo na linafanyiwa kazi. Niwaombe kuwa na subra ili muda ukifika basi mtapata majibu ya maamuzi ya Serikali.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi ya swali la nyongeza. Kwa kuwa kanuni ya 10(3) ya kifungu 37A cha Sura ya 290 ya Fedha za Serikali za Mitaa inayohusu asilimia 10; imeitaka Mamlaka ya Serikali za Mitaa kukabiliana na mkopaji namna bora ya kurudisha fedha zile za mkopo. Je, Serikali haioni kwamba Kanuni hii inatoa loophole kwa Watendaji kuingiza mambo kinyume cha utaratibu na hawaoni haja kuweka muda wa marejesho kulingana na kiwango cha fedha ambacho kikundi kile kitakuwa kimekopa? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Kanuni ya Fedha ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa na Kanuni ile inayoelekeza mikopo ya asilimia 10 imeweka nafasi ya Watendaji katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa kukubaliana na vikundi vya ujasiriamali kuhusu utaratibu na muda wa marejesho ya mikopo hiyo. Dhamira yake ilikuwa, kwa kuwa mazingira haya ya wakopaji yanatofautiana sehemu moja na nyingine, lakini pia uwezo wa vikundi kurejesha unatofautiana kutoka kikundi kimoja na kikundi kingine, kwa hiyo, tunapokea ushauri wake. Tutafanya tathmini kuona uwezekano wa kuweka standard ya muda wa marejesho kwa kiasi fulani na pia tutaboresha njia hiyo kuhakikisha kwamba zile fedha hazipotei. Ahsante. (Makofi)
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, majibu yanatuonesha kwamba yapo malalamiko mengi sana ya fedha hizi takribani shilingi bilioni 60 ambazo zinarudi kila mwaka zinapatikana kutokea kwenye fungu hili la 10% na mifano imeoneshwa; Dar es Salaam kwenye Wilaya mojawapo tayari kuna ubadhirifu mkubwa sana wa fedha hizi: -

Je, Serikali haioni ni wakati sasa wa kupeleka ukaguzi maalum kwa nchi nzima ili tupate tathmini ya kweli? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Kibamba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kumekuwa na malalamiko ya baadhi ya maeneo nchini kote kuhusiana na matumizi ya fedha za 10% na Serikali kama ambavyo Waziri wa Nchi, Mheshimiwa Bashungwa ametoa maelezo mwanzoni, ni kwamba tunafanya tathmini ya kuona wapi kuna mafanikio, maeneo gani yana changamoto, na changamoto ni zipi; ili sasa baada ya tathmini hiyo, tuwe na direction ambayo itatuwezesha kuwa na fedha ambazo zinaleta tija kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kutakuwa na sababu ya kutazama uwezekano wa kufanya ukaguzi maalum tutalifanya kwa sababu kazi ya Serikali ni kudhibiti fedha hizo ili ziweze kuleta tija kwa watarajiwa. Kwa hiyo, tumelichukua wazo hilo na tutaendelea kulifanyia kazi. Ahsante. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ninashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza ni, kwa sababu wanawake au makundi haya kwa sasa hivi yanapata mkopo kwa kiwango kidogo sana kiasi kwamba mkopo huo hauwasaidii.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kiwango hicho kutoka milioni mbili na laki tano kwa kila kundi mpaka milioni kumi ili waweze kufanya vizuri kwenye biashara zao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali sasa ina mpango gani wa kuwajengea mafunzo na uwezo kabla makundi haya hayajapewa mkopo?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, makundi haya ambayo ni ya wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu yanakopesha asilimia 10, kwa maana ya 4:4:2, lakini kiwango cha ukopeshaji hakijaainishwa, inategemea aina ya shughuli ya ujasiriamali, si kila kikundi kinakopesha milioni mbili na laki tano. Kila kikundi kinakopeshwa kuliangana na uhitaji wa biashara yao, lakini pia uwezo wa kurejesha fedha zile baada ya kukopeshwa.

Mheshimiwa Spika, na Serikali imetoa tamko kwamba tunahitaji kuona vikundi vya wajasiriamali wanakopeshwa fedha zenye kiwango ambacho kinaleta tija ya kuwawezesha kutoka hatua moja kwenda hatua nyingine badala ya kutoa fedha kidogokidogo ambazo kwanza haziwawezeshi kiuchumi, lakini pili inakuwa ni changamoto kuzirejeshwa. Kwa hiyo, maelekezo haya yametolewa, na Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ameelekeza na sisi Ofisi ya Rais TAMISEMI tunalitekeleza.

Mheshimiwa Spika, na nichukue nafasi hii kutoa maelekezo kwa halmashauri zote kuhakikisha kwamba wanatoa fedha yenye tija badala ya kutoa fedha kidogo kidogo kwa vikundi vya wajasirimali.

Mheshimiwa Spika, mpango wa mafunzo umewekwa vizuri. Maafisa Maendeleo ya Jamii katika hamashauri zetu wanawajibika kwanza kuwajengea uwezo kwa maana ya mafunzo pamoja na kuwatembelea na kuhakikisha kwamba wanafanya biashara zao, na zoezi hili ni endelevu. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Waliokuwa Bungeni kabla yetu waliona busara kwamba asilimia 10 iende kwa wanawake, na baadae sasa makundi yale yalivyobainika ikaonekana ile ile asilimia 10 igawanywe kwa walemavu na vijana.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wanawake wakabaki na ile asilimia 10 na yale makundi mengine yakapatiwa asilimia yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Mikopo ya Ujasiriamali iliyopitishwa na Bunge hili mwaka 2019 inaelekeza asilimia 10 kwa ajili ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Ni kweli kwamba tulianza na asilimia 10 kwa wanawake, lakini baada ya tathimini ya makundi yenye uhitaji wa kujengewa uwezo wa ujasiriamali yaliongezeka makundi ya vijana pamoja na makundi ya watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, makundi haya yote ni muhimu kujengewa uwezo katika jamii yetu. Hata hivyo tunachukua wazo lake kuendelea kufanya tathmini. Lakini kabla hatujafikia hatua hiyo tunafanya tathmini ya ufanisi, changamoto na mafanikio ya hii asilimia 10, kwa maana ya 4:4:2, na baada ya hapo tutaona maeneo gani tuboreshe ili tuweze ku-accommodate mawazo ya Waheshimiwa Wabunge. Ahsante sana.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kuna zile fedha za marejesho za miaka iliyopita ambazo huwa zinajeshwa ambazo inaonekana kwamba kila halmashauri inakuwa na utaratibu wake.

Mheshimiwa Spika, nini kauli ya Serikali kuhusiana na hizi fedha zinazorejeshwa ambazo zingeweza kuongeza kiasi cha wanaokopa wakapata fedha nyingi zaidi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimia Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya fedha za marejesho ya asilimia 10 zimefunguliwa akaunti zake mahsusi, kwa hiyo wajasiriamali wanaporejesha fedha zile zinatakiwa kuingizwa kwenye akaunti mahsusi ya marejesho ya mikopo ya asilimia 10. Akaunti ile ni revolving fund, maana yake baada ya kurejeshwa zinatakiwa kuendelea kuwakopesha vikundi vya wajasiriamali. Kwa hiyo, matarajio ya Serikali ni kwamba akaunti zile kila baada ya mwaka wa fedha zitakuwa zinaendelea kuongezeka na kutakuwa na fedha za kutosha zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie nafasi hii kumhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ilitoa maelekezo, na hakuna halmashauri inayotakiwa kwenda kinyume na maelekezo haya. Nitoe wito kwamba halmashauri zote ni lazima zihakikishe kwamba akaunti za marejesho zinafanya kazi, na fedha zile zikirejeshwa ziendelee kukopesha wajasiriamali wengine.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa muda huu wa maswali madogo mawili ya nyongeza. Ninaishukuru sana Serikali kwa fedha hizo zilizotolewa, na hivi karibuni tulipata milioni 300, nasema ahsante kwa Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa maana ya Mwamkulu fedha zilizotolewa zina uwezo wa kujenga OPD. Ni lini Serikali itatuongeza fedha ili tuweze kumalizia majengo mengine?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Kituo cha Afya cha Ilembo kilibahatika kupata fedha shilingi milioni 400, lakini fedha zile hazikulenga vifaa tiba. Ni lini Serikali itatusaidia fedha ili tuweze kununua vifaa tiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee shukrani nyingi za Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya wananchi wa Manispaa ya Mpanda ambazo amezielekeza kwa Serikali yetu inayochapa kazi, chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan. Na ni kweli, hakuna jimbo ambalo halijapata vituo vya afya na zahanati. Kazi inaendelea na tunaona wananchi wetu wananufaika na miradi hii ya afya.

Mheshimiwa Spika, Kituo hiki cha Afya cha Mwamkulu kimepewa milioni 250, na maelekezo ni kujenga majengo matatu. Jengo la OPD, maabara pamoja na kichomea taka. Kwa hiyo milioni 250 si ya kujenga OPD peke yake, na hiyo ni standard kwa milioni 250 zilizotolewa nchini kote. Awamu ya pili tutapeleka fedha tena kwa ajili ya kikamilisha majengo yaliyobaki yakiwemo wodi, majengo ya upasuaji na majengo mengine muhimu.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la vifaa, Serikali imeweka utarartibu, kuanza baada ya kukamilisha miundombinu hiyo, kwa awamu tutapeleka fedha kwa ajili ya kununua vifaa tiba ili kuwezesha vituo vyetu kufanya kazi vizuri zaidi. Ahsante.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Mwaka 2017/2018 Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuwa anazindua Siku ya Ushiriki wa Afya Duniani katika Jimbo la Ushetu katika Halmashauri ya Ushetu, Kata ya Ulowa, aliwaaahidi wananchi kuwajengea kituo cha afya, lakini hadi leo ni miaka mitano kituo hicho hakijaanza kujengwa.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Kituo Cha Afya kwa wananchi wa Ulowa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Cherehani, Mbunge wa Jimbo la Ushetu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ahadi zote za viongozi wetu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji, kikiwepo Kituo cha Afya katika Kata ya Ulowa. Kwa hiyo, ninaomba nimhakikishie kwamba Serikali imechukua mahitaji na ahadi hii, na tunatafuta fedha, wakati wowote kupitia fedha za tozo tutaleta pale milioni 250 ili Kituo cha Afya cha Ulowa kianze kujengwa. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ninaomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya pale Moshi Mjini, kwa sababu ilishapitishwa kwenye bajeti na wengine wameshapata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo Mbunge, wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 14 kwa ajili ya hospitali za halmashauri 28 katika hamashauri ambazo hazina kabisa hospitali za halmashauri ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba ndani ya mwaka huu wa fedha lengo la Serikali ni kuleta fedha hiyo, milioni 500, ili kazi ya ujenzi iweze kuanza. Ahsante.
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba imeanza ujenzi wa Kituo cha Afya kwa mapato ya ndani, na jengo la la wagonjwa wa nje (OPD) limekamilika. Sasa ni nini mpango wa Serikali kuisaidia halmashauri hiyo kukamilisha majengo yaliyobaki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godwin Kunambi, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa ujenzi wa vituo vya afya unahusisha nguvu za wananchi katika michango yao na kujenga vituo hivyo. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwanza kuwapongeza sana wananchi wa Jimbo hili la Mlimba, ambako Mheshimiwa Kunambi ndiye Mbunge, kwa kazi nzuri na kubwa ambayo wameifanya ya kujenga kituo cha afya. Nimhakikishie, kwa awamu tutatafuta fedha ili kuhakikisha kwamba tunakamilisha miundombinu ambayo inabaki.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, licha ya majibu mazuri niliyoyapata kutoka Serikalini, naomba kuuliza maswali mengine madogo mawili.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, kuna mkakati gani wa kutatua tatizo la upungufu wa dawa unaojitokeza kwenye Mkoa wa Morogoro?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, kuna mkakati gani wa Serikali kukabiliana na changamoto zinazojitokeza kwenye upande wa chanjo, hasa chanjo za akina mama wajawazito na watoto wachanga ambao unajitokeza Mkoani Morogoro, hususan Manispaa ya Morogoro? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa kutatua changamoto za upatikanaji wa baadhi ya dawa katika vituo vyetu, kwanza Serikali imeongoza bajeti ya dawa inayopelekwa Bohari ya Dawa (MSD) kwa zaidi ya mara saba na hivi sasa Serikali ilishapeleka MSD takribani shilingi bilioni 300 kwa ajili ya dawa, lakini pia mpango umewekwa kupeleka angalau kila mwezi shilingi bilioni 15 ili kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana.

Mheshimiwa Spika, mpango wa pili ni kuhakikisha kwamba dawa zinazonunuliwa na kupelekwa kwenye vituo vyetu zinatumika ipasavyo na kuepuka matumizi mabaya ya dawa kwa maana ya upotevu wa dawa, lakini pia na fedha zitokanazo na uchangiaji wa huduma za dawa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na mkakati wa kukabiliana na changamoto za chanjo katika Mkoa wa Morogoro. Kwanza naomba nipokee hoja ya Mheshimiwa Mbunge na baada ya hapa nitajifunza changamoto ni zipi ili tuweze kuona namna ya kwenda kuzitatua. Lakini jambo la muhimu ni kwamba ni haki ya msingi ya watoto na akina mama kupata chanjo na Serikali imeendelea kuhakikisha chanjo zinapatikana ili kuboresha huduma za wananchi. Ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali imejenga hospitali za Halmashauri katika Halmashauri za Wilaya za Mbulu na Babati, na kwa sehemu kubwa hospitali hizo zimekamilika. Sasa Serikali inapeleka lini watalaam kulingana na ikama, lakini vilevile na vifaatiba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ni hatua moja ya kusogeza huduma za afya karibu zaidi na wananchi, lakini hatua ya pili ni kupeleka watendaji, kwa maana ya watumishi wa kada mbalimbali za afya, vifaatiba, lakini pia na kupeleka dawa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya ujenzi wa hospitali hizo mpango wa Serikali ni kuendelea sasa kupeleka wataalam ili huduma ziendelee kutolewa kwa wananchi.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kuna upungufu mkubwa sana wa kada ya uuguzi na madaktari katika vituo vyetu vya afya na zahanati zetu, na kwa kuwa tunaona kuna wimbi kubwa la wastaafu wa kada hizo wanaopewa barua za kustaafu kila siku.

Je, Serikali haioni umefika wakati sasa wa TAMISEMI kukaa na Wizara ya Utumishi ama kuwaongezea mkataba watumishi hawa ama kutoa fursa ya kutoa ajira ku-replace hawa watu ambao wanaondoka kwenye ajira kwa sababu bado wanakuwa kwenye bajeti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwa na upungufu wa watumishi kwenye vituo vyetu, lakini jitihada za wazi za Serikali zimeendelea kuonekana, kwanza kwa kuajiri watumishi katika vituo hivyo. Kwa mwaka uliopita Serikali iliajiri zaidi ya watumishi 2,726 wa kada za afya na kuwasambaza nchini kote.

Mheshimiwa Spika, lakini upungufu huu wa watumishi pia unatokana na kasi kubwa ya Serikali ya kujenga zahanati, vituo vya afya na hospitali. Kwa sababu idadi sasa ya vituo hivyo imekuwa kubwa na automatically upungufu wa watumishi unaonekana. Kwa hiyo ni hatua nzuri sana kwanza ya kusogeza huduma kwa wananchi, lakini hatua ya pili ni kupeleka watumishi hao.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kuwaongezea mkataba waliostaafu; tunafikiri ni busara kwa sababu kuna vijana wengi wamehitimu masomo ya utabibu, ya uuguzi, ni vyema wakaajiriwa badala ya kuongeza mikataba ya wale ambao wamefika umri wa kustaafu kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, tutaendelea kuhakikisha kwamba fursa za ajira zikitokea vijana wanajiriwa kwenda kupunguza mapengo ya watumishi katika kada za afya. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza mimi nimpongeza Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri na tunakiri kabisa kwamba wameleta fedha.

Nina maswali mawili ya nyongeza; la kwanza, mwaka 2017 Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja katika Kata ya Goweko, Kijiji cha Imalakaseko kulikuwa na wodi ambayo walianzisha wananchi, aliahidi ataleta shilingi milioni 80 tangu mwaka 2017 mpaka leo hazijafika? Lakini vilevile aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI Selemani Jaffo mwaka 2019 alikuja katika Kata ya Igalula wodi ipo pale wananchi walianzisha aliahidi ataleta fedha mpaka leo, halikadhalika na kata zingine.

Mheshimiwa Spika, nataka nijue nini kauli ya Serikali kulinda ahadi za viongozi endapo wanatoa ahadi na hazitekelezeki kwa wakati?

Swali langu la pili ni mkakati gani Serikali sasa itatoa kumaliza maboma yote ili kuwatia nguvu na moyo wananchi ambao wamejitoa kuisaidia Serikali? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daud Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali ni kwamba ahadi zote za Viongozi wetu wa Kitaifa ni lazima zitatekelezwa na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi hii ya milioni 80 ya Mheshimiwa Waziri Mkuu tutapeleka fedha hizi kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha 2021/2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu na suala la mkakati wa umaliziwaji wa maboma katika jibu langu la msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali kwanza imepeleka fedha nyingi kwenye maboma, lakini kuyatambua maboma yote zaidi ya 1700. Lakini tatu tunatafuta fedha na kupeleka kwa awamu kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo.

Mheshimiwa spika, kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba mkakati wa Serikali uko thabiti na tutaendelea kuyakamilisha maboma hayo kupitia mapato ya ndani na mapato ya Serikali Kuu. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, pamoja na jibu zuri la Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza ni kwamba, pamoja na uchakavu wa hospitali hii, lakini hatuna gari la wagonjwa: Je, ni lini Serikali italeta gari la kubebea wagonjwa (ambulance)?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Ni lini Waziri atafanya ziara katika hospitali hii ya Wilaya ya Mpwapwa ili ajionee hali halisi ya hospitali ile? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mwaka huu wa fedha atapata gari la wagonjwa kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya katika Halmashauri ya Mpwapwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, nilifanya ziara mwezi wa Nne mwaka huu katika Hospitali ya Mpwapwa, lakini nipo tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge kwenda kufanya ziara tena kuona namna ya kuboresha huduma pale. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nini mpango wa Serikali kupeleka vifaa tiba kwenye zahanati zilizokamilishwa kwa nguvu za wananchi hasa katika Vijiji vya Mundarara, Loremeta, Gelai Lumbwa, vilivyopo katika Wilaya ya Logindo, Mkoa wa Arusha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga Shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba katika vituo 530 zikiwemo hizi zahanati ambazo zimejengwa kwa nguvu za wananchi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri au Wilaya katika Jimbo la Kilombero unaenda kwa kusuasua: Je, Serikali inawahakikishia nini wananchi wa Jimbo la Kilombero kwamba hospitali hiyo ya Halmashauri itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asenga ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilombero kuhakikisha anatumia fedha za Serikali zilizoletwa kwa ajili ya kujenga hospitali hiyo, na hospitali hiyo ikamilike kwa wakati kama mpango kazi ulivyo. Nasi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutafuatilia kuona utekelezaji huo. Ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya swali la nyongeza. Hospitali ya Wilaya ya Kilwa maarufu kama Kinyonga iliyopo Kilwa Kivinje ni chakavu, lakini imeidhinishiwa fedha shilingi milioni 900: Lini Serikali itapeleka fedha hizo ili ukarabati ufanyike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hospitali chakavu kama hospitali ya Wilaya ya Kilwa maarufu “Kinyonga”, imetengewa Shilingi milioni 900 na katika mwaka huu wa fedha Serikali inaendelea kutafuta fedha ili tupeleke katika hospitali hiyo kwa ajili ya ukarabati. Ahsante. (Makofi)
MHE. MATHAYO D. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Vudee na Kata ya Mshewa katika Jimbo la Same Magharibi, ni miongoni mwa Kata za kujengewa vituo vya afya vya kimkakati: Je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata ya Vudee na Kata ya Mshewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mathayo David Mathayo, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mbunge kwamba Serikali iliainisha kata zote za kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya na tutakwenda kujenga vituo vya afya hivyo kwa awamu ikiwemo kata hizi za kimkakati katika Jimbo la Same Magharibi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wilaya ya Biharamulo, tuna ujenzi wa hospitali ya Wilaya pale, lakini ujenzi ule umekwama kwa muda mrefu kwa sababu ya pesa iliyorudishwa Shilingi milioni 204. Hii fedha nimeisema mbele ya Rais akiwa Biharamulo tarehe 8 Juni, na TAMISEMI wakaahidi kwamba wanakwenda kuifuatilia: Ni lini sasa fedha hii italetwa ili tuweze kukamilisha kwa sababu kila kitu kiko tayari pale isipokuwa fedha hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Mbunge amefuatilia sana suala ya fedha hizi na ameshauliza hapa. Tulikubaliana na Hazina kwa maana ya Wizara ya Fedha, fedha zile ziweze kurejeshwa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia sisi na Wizara ya Fedha, tuhakikishe fedha zinakwenda kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Halmashauri ya Mji wa Bunda, imeanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri kwenye Kata ya Bunda Store, na Serikali ilitenga Shilingi milioni 500: Kuna mkakati gani wa kutenga fedha kila mwaka wa fedha ili ile hospitali iweze kukamilika haraka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, dhamira ya Serikali ni kuendelea kutenga fedha kila mwaka wa fedha, ndiyo maana tulipeleka Shilingi milioni 500 na kila mwaka wa fedha tutatenga Shilingi milioni 500 au zaidi kuhakikisha Hospitali ya Mji wa Bunda pia inakamilika. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri, lakini kwa kuwa mtendaji ni mmoja na watendaji wa vijiji wako wawili tu, kata ni kubwa, ina vijiji 16: Ni lini Serikali itaongeza watendaji kwa ajili ya kata hiyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kutokana na mazingira magumu ya kata hiyo, vijiji 16 na mazingira magumu: Ni lini Mtendaji wa Kata ya Katumba anaweza kupata usafiri kwa ajili ya kufanya kazi kwa ufanisi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua kwamba kata hii ni kubwa, ina vijiji 16 na inahitaji nguvu zaidi kwa watendaji wa kata kuhakikisha kwamba wanatoa huduma na pia watendaji wa vijiji. Naomba nilichukue jambo hili, tutalifanyia kazi na nitawasiliana naye kuhakikisha kwamba kata hii inaongezewa nguvu ya watendaji. Ahsante.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa mahitaji makubwa ya wananchi ni kupata vitongoji vipya na vijiji vipya; na kwa kuwa mchakato huu haueleweki sana kwao, sisi tunalalamikiwa: Je, Serikali ina utaratibu gani sasa wa kugawa vijiji na vitongoji na mitaa ili kurahisisha huduma kwa wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zacharia Issaay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna mahitaji ya kugawa vijiji, vitongoji, kata na mara nyingine hata Halmashauri katika nchi yetu, lakini kama nilivyotangulia kujibu kwenye maswali ya msingi kwamba kipaumbele chetu sasa Serikali ni kuboresha kwanza miundombinu katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, utaratibu ni kwamba wananchi wanafanya vikao vyao vya Halmashauri za Kijiji na kwenda DCC na RCC na baadaye kuwasilisha maombi Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo, namwombe Mheshimiwa Mbunge waanze taratibu hizo za kisheria wakati tukisubiri maamuzi ya Serikali kuja kugawa maeneo mengine ya kiutawala. Ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kata ya Rungwe Mpya iliyoko Jimbo la Kasulu Vijijini ina idadi kubwa ya watu wengi sana: Je, ni lini Serikali itakubali kuigawa kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itagawa kata hizo baada ya kuwa tayari imeshaboresha miundombinu kwenye maeneo ya utawala yaliyopo sasa. Tuna kata nyingi na vijiji ambavyo bado vinahitaji uboreshaji. Kwa hiyo, baada ya hapo tutakwenda pia kutazama Kata hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja. Ahsante.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Mlowo ni moja kati ya kata kubwa sana katika Mkoa wetu wa Songwe: Ni hatua zipi Serikali imefikia katika mchakato wa kuigawa kata hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kata ya Mlowo ni moja ya kata kubwa, lakini utaratibu ni kwamba, endeleeni na taratibu za kuwasilisha maombi kwa mujibu wa taratibu za ugawaji wa maeneo ya utawala. Hata hivyo kipaumbele kwa sasa ni kuhakikisha tunaboresha miundombinu kwenye kata zilizopo kabla hatujakwenda kugawa kata hizi nyingine. Ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri naomba niulize maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza kwa kuwa magari yaliyonunuliwa ni 195 na halmashauri ziko 184 nchini; je, kati ya haya magari yaliyobaki moja litakwenda kwenye Kituo cha Afya cha Gidas?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa mahitaji ya wahudumu wa afya katika kituo hicho ni 32 na waliopo sasa ni nane tu; je, Serikali iko tayari kuongeza wahudumu wa afya ili kuboresha huduma za afya kwenye kituo hicho? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba magari yatakayonunuliwa ni 195 lakini tuna halmashauri 184 na tutazama zile halmashauri au vituo ambavyo viko mbali zaidi maeneo ambayo ni hard to reach tutawapa kipaumbele kuwapa gari zaidi ya moja katika halmashauri hizo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hoja ya Kituo cha Afya cha Gidas amesema kwa muda mrefu, tutakwenda kuona uwezekano wa kuwatafutia gari ili tuweze kuondoa changamoto ya wananchi katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kuhusiana na watumishi ni kweli tunachangamoto ya upungufu wa watumishi, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ameona Serikali imeendelea kuajiri watumishi na kuwapeleka kwenye vituo vya afya, tutahakikisha tunaendelea hivyo kwa awamu na tutatoa kipaumbele cha afya hicho cha Gidas. Ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, na matatizo ya magari ya kubebea wagonjwa katika vituo vya afya; je, ni lini Serikali itapeleka magari hayo katika Kituo cha Afya cha Kisolya na kile cha Kasuguti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, magari ya wagonjwa yatapeleka kwenye halmashauri zote 184 nchini kote na sasa ni maamuzi ya halmashauri kuona kipaumbele katika halmashauri yao ni kituo kipi cha afya ambacho kina uhitaji zaidi wa gari la wagonjwa.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Arumeru kuna gari moja tu la kubebea wagonjwa; je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka gari la ziada katika Wilaya ya Arumeru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zaytun Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kati ya Oktoba na Novemba mwaka huu gari moja jipya la wagonjwa litapelekwa katika Halmashauri hii ya Arumeru. Ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kuna halmashauri ambazo zina hospitali mbili za wilaya ikiwemo na halmashauri ninayotoka mimi ya Geita. Sasa Serikali itapeleka magari mawili kwa sababu ukipeleka gari moja linakuwa na mgongano wa hoja kwa sababu kuna hospitali mbili na Wabunge wawili tofauti.

Je, Serikali ipo tayari kupeleka magari mawili katika Halmashauri ya Geita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, magari yanapelekwa kwenye halmashauri na halmashauri ziko 184 magari yako 195. Kwa hiyo, kila halmashauri ikiwepo halmashauri ya Mji wa Geita lakini pia Halmashauri ya Wilaya ya Geita watapata gari moja moja, ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kumekuwa na ahadi ya muda mrefu sana kupeleka gari ya wagonjwa katika Kituo cha Afya Mlola. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo kupeleka gari Kituo cha Afya Mlola?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shabani Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, halmashauri ya Lushoto itapewa gari la wagonjwa jipya kati ya Oktoba na Novemba mwaka huu, kwa hivyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Mkurugenzi waone uwezekano wa kupeleka gari hili katika kituo cha afya cha kipaumbele kikubwa zaidi ikiwemo hicho ambacho amekitaja. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kutokana na umbali wa Kituo cha Afya Nanjilinji kutoka Makao Makuu ya Wilaya, lakini pia kutoka Hospitali ya Wilaya ya Kinyonga; je, Serikali itakubaliana nami kwamba upo umuhimu wa kupeleka gari la wagonjwa kwa umuhimu wake na upekee wake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikweli Kituo cha Afya Nanjilinji kiko mbali lakini kinahudumia wananchi wengi na Mheshimiwa Mbunge amekifuatilia na tumekubaliana kwamba katika vituo ambavyo vitapewa magari ni pamoja na Kituo cha Afya cha Nanjilinji.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Simbayi na Tarafa ya Basuto katika Jimbo la Hanang tuna changamoto kubwa sana kwanza ya umbali na hakuna gari la wagonjwa; je, ni lini Serikali sasa itapeleka magari ya wagonjwa katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Abdukarimu Halamga, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tarafa hizi ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja alikwishazileta na pia kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge Hhayuma wamekuwa wakishirikiana kwa karibu sana na kuona wananchi wa Hanang wanapata huduma hizi na nimhakikishie tu kwamba Mheshimiwa Mbunge tumeshafanya tathinini ya kuona uwezekano wa kupeleka la wagonjwa lakini gari moja la wagonjwa jipya litaletwa Hanang ili muweze kupeleka katika tarafa hizo, ashante.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa teknolojia inabadilika kila wakati; je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha kuwa hizo CCTV camera na alarm systems zinahuishwa kila wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa Serikali imeshachukua hatua ya kuanza kufunga mifumo ya kutambua na kudhibiti majanga kwa majengo mapya; je, Serikali inatoa kauli gani kwa majengo ya zamani? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumeshaweka mpango wa kitaifa wa kudhibiti majanga hususani majanga ya moto na tayari tumeshaanza kufanga katika maeneo hayo na tunafahamu kwamba teknolojia ni dynamic, inabadilika mara kwa mara na sisi tumejipanga kuhakikisha tunahuisha mifumo hii ya udhibiti lakini pia ya kutambua changamoto za majanga ikiwepo moto kila mara.

Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na nimpongeze kwa ufuatiliaji wake mzuri kwamba Serikali imeweka mfumo ambao utakuwa mara kwa mara unapitia na ku-update mifumo hiyo ili iweze kufanya kazi vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu majengo ya zamani ni kweli kwamba mifumo hii sasa kwenye majengo mapya imekuwa sehemu ya michoro kuhakikisha kwamba inazingatia uwepo wa vifaa na miundombinu hiyo. Lakini tumetoa maelekezo katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa katika mikoa kote nchini kuhakikisha katika majengo yale ya zamani yakiwemo masoko, Ofisi za Serikali na maeneo kama hayo wanafunga mifugo ya kutambua na kudhibiti majanga ya moto, ahsante.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Kama alivyosema, kituo hiki ni kikongwe, hakuna ufinyu wa eneo. Kwa kuwa kutoka kituo hiki mpaka kituo kingine cha hadhi kama hii ni kilomita 50: Serikali haioni sasa ni vizuri kwa dharura ikawaonea huruma watu wa Bungu, angalau kuwajengea jengo la upasuaji au jengo la mama na mtoto ili kuwasaidia wananchi hasa akina mama na watoto? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wakati tukiwa tunasubiri hizo fedha na taratibu nyingine zote zikamilike, wananchi hawa wanateseka: Ni lini Serikali itapeleka gari la uhakika la wagonjwa ili kuwasaidia wananchi wa Bungu, kutoka Bungu kwenda mpaka Korogwe Mjini kilomita 50 kupata matibabu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo hiki cha Afya cha Bungu kiko katika eneo lenye ukubwa wa ekari mbili, lakini standards zetu za vituo vya afya ni angalau ekari kumi na Serikali imefanya tathmini kwa aina ya uchakavu mkubwa wa kituo kile cha afya, haitakuwa na tija kuweka fedha za kukarabati kituo kile. Ni vema kujenga kituo cha afya ambacho kitaendana na ramani za kisasa. Bahati nzuri kituo hicho kinajenga ndani ya Kijiji kile kile cha Bungu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge kwamba kituo cha afya kitajenga katika kijiji kile na Halmashauri itaanza kutenga fedha katika mwaka ujao wa fedha mpaka kitakapokamilika.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kununua magari ya wagonjwa. Niwahakikishie Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe pia itapelekewa gari la wagonjwa ndani ya mwezi ujao. Ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, kwa kuwa hivi sasa halmashauri zimejenga zahanati nyingi na vituo vingi lakini maeneo mengi unakuta anayetibu ni muuguzi badala ya mganga. Ni lini Wizara itafanya tathmini kuona kwamba katika kila zahanati na vituo vya afya kuna idadi ya watumishi wanaotakiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Constantine Kanyasu, Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilishafanya tathmini na tunafahamu upungufu wa watumishi katika vituo vyetu na kweli baadhi ya zahanati bado zinahudumiwa na wauguzi bila kuwa na madaktari na waganga. Lakini kama ambavyo Serikali imeendelea kuweka mpango ni kuendelea kuajiri watumishi, mwaka huu watumishi wameajiriwa zaidi ya 7,600 lakini tutaendelea kuajiri kwa awamu ili kuhakikisha watumishi wanapelekwa kwenye zahanati zetu ahsante.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona, Kituo cha Afya cha Mtanila, pamoja na Kituo cha Afya cha Kata ya Lupa ni vituo vya afya vya muda mrefu na vimechakaa sana. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kukarabati vituo hivi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasaka, Mbunge wa Jimbo la Lupa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilifanya tathmini ya vituo vya afya, hospitali na zahanati zote chakavu sana nchini kote na tumeweka mpango wa kuanza kukarabati kwa awamu. Kwa mfano kwa mwaka huu tutakarabati hospitali 19 chakavu za wilaya, lakini tutakwenda pia kukarabati vituo vya afya chakavu na zahanati chakavu kwa awamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kutenga fedha kwa awamu kwa ajili ya vituo hivyo vya afya.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza niishukuru Serikali kwa majibu hayo lakini nimkumbushe tu Mheshimiwa Waziri kwamba vituo hivi vya kimkakati tulikubaliana, pamoja na kujengwa Makao Makuu ya Kata, lakini pia vijengwe kwenye kata zile za mbali. Kwa hiyo, Kata ya Ukata iko mbali sana na hiki kituo cha Mkumbi. Kwa hiyo, nini maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali ilipeleka fedha milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Mapela na mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali ilitenga fedha kwa ajili ya vifaa tiba Shilingi milioni 320, lakini mpaka leo hii vifaa tiba katika kituo hiki cha afya havijafika. Sasa nataka kujua fedha hizi ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Kituo hiki cha Mkundi, Matiri, pamoja na Muungano, sasa hivi vimeshakamilika. Ni lini sasa tutapeleka watumishi pale ili vianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ilitoa mwongozo wa kujenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati, vigezo vikiwa kwanza idadi ya wananchi katika eneo husika, lakini pili, umbali wa kituo kile kutoka kituo cha karibu zaidi au hospitali ya karibu zaidi. Kwa hiyo, ukitoa kata yoyote ambayo inakidhi vigezo hivyo ina sifa ya kuwa kata ya kimkakati kwa ajili ya kituo cha afya. Kwa taarifa tulizonazo bado idadi ya watu sio kubwa sana, kwa hivyo inakosa ile sifa kuwa kituo cha afya cha kimkakati kwa maana ya idadi ya wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, shilingi milioni 400 zilipelekwa katika kituo cha afya alichokitaja Mheshimiwa Mbunge na milioni 320 za vifaa tiba tayari zimepelekwa Bohari Kuu ya Madawa (MSD) kwa ajili ya kuleta vifaa hivyo. Tunaendelea kushikirikiana na Wizara ya Afya, kuhakikisha vifaa hivyo vinaletwa mapema iwezekanavyo ili huduma za afya zianze kutolewa katika kituo kile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na hivi vituo vitatu vilivyokamilika, kwanza tumshukuru Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuleta fedha nyingi kukamilisha vituo vya afya vitatu na nimhakikishie Mbunge kwamba mpango wa ajira kwa watumishi kwa awamu ni kuhakikisha kwamba tunaleta watumishi kwenye vituo hivyo pia ili huduma zianze kutolewa.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa katika ngazi ya Wizara, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo na Uvuvi, ni Wizara mbili tofauti zenye majukumu tofauti. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 ndiyo Wizara zilizopewa fedha nyingi za miradi, watendaji wa Wizara hizi wako katika halmashauri. Je, sasa kwa mfano Wizara moja inapotoa maelekezo halmashauri na kwenda kusimamiwa na mkuu wa idara nyingine, mfano Wizara ya Kilimo, kutoa maelekezo kwa Mkuu wa Idara ya Mifugo, je, hakutarudisha ufanisi wa utendaji wa kazi hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Idara hizi za Kilimo na Mifugo katika halmashauri ndizo zinazotegemewa kwa mapato ya ndani, sasa kumwachia majukumu mkuu wa idara moja kusimamia ukusanyaji wa mapato ya kilimo, mifugo na uvuvi, je, hakutaathiri ukusanyaji wa mapato katika halmashauri hizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Wizara ya Kilimo na Wizara ya Mifugo ni Wizara mbili tofauti kwa ngazi ya Wizara, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara zikiwa tofauti haimaanishi kwamba coordination ya kuwatumia na kuwaelekeza Wakuu Idara katika Halmashauri inakwama. Halmashauri zetu zinatofautiana, kuna halmashauri ambazo zinashughuli nyingi zaidi za mifugo, kuna halmashauri nyingi zaidi ambazo ni za kilimo. Wakuu wa Idara wa Halmashauri hizo itazingatiwa halmashauri ina idadi kubwa zaidi ya shughuli gani, kama ni za kilimo, Mkuu wa Idara atakuwa ni Afisa wa Kilimo. Kama ni mifugo Mkuu wa Idara atakuwa ni mtaalam wa masuala ya mifugo na coordination ya Serikali ni moja mpaka chini bila kujali utofauti wa Wizara katika ngazi ya kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na mapato ambayo yanakusanywa kutoka Idara ya Kilimo na Idara ya Mifugo, ikumbukwe kwamba wataalam wote wa mifugo wanaendelea kuwepo na Wakuu wa Idara kwa maana ya wataalam wetu wa kilimo wanaendelea kuwepo, kinachotofautisha ni mkuu wa idara lakini ataendelea kuwaratibu na kuwasimamia wataalam katika ukusanyaji mapato katika kusimamia shughuli za kilimo na mifugo kwa muktadha huo. Ahsante sana.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nasikitika kidogo kwa majibu ambayo Serikali imetoa, anakubaliana kwamba uhakiki umekamilika tangu 2015 na sasa ni miaka nane mpaka leo watumishi wale hawajalipwa hata shilingi moja. Hata hivyo, kinachosikitisha zaidi, wapo waliostaafu lakini pia wapo ambao wamekufa. Nataka kujua nini hatima ya hao waliostaafu na hao waliokufa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kulipa madai yoyote ya watumishi lazima uhakiki kujiridhisha zaidi ya shaka kwamba wanaodai wanadai kiwango halali na wanastahili kulipwa malipo hayo. Ni kweli kwamba uhakiki ulianza mwaka 2015/2016, lakini kuna dosari nyingi za madai zilionekana miongoni mwa wale ambao walitakiwa kulipwa na Serikali isingeweza kuwalipa kabla ya kujiridhisha kwamba kiasi ambacho wanadai wanatakiwa kulipwa. Kwa hiyo, baada ya Mkaguzi wa Ndani kutoka Makao Makuu kufanya ukaguzi, ikaonekana madai yale yameshuka na ndiyo maana yamechelewa kuanza kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba mwaka ujao inatengwa fedha, lakini kila mwaka tutatenga fedha kuhakikisha wote waliostaafu, walioko kazini na hata ambao wametangulia mbele za haki wanalipwa kwa kupitia wale ndugu ambao ni wategemezi wa hao waliotangulia mbele za haki.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini mpango wake wa 2024/2025 ni mbali sana. Ione uwezekano wa kurudisha kati 2023/2024. Maswali mawili ya nyongeza ni haya: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Mgama, kipo kituo cha afya na wananchi walishajenga msingi wa wodi, sasa uwezo wao wa kuendelea kujenga ni mdogo: Je, ni lini Serikali itatusaidia kuleta fedha ili tujenge wodi ili wananchi wa vijiji 12 wanaohudumiwa hapo wapate huduma?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Pamoja na kwamba umesema Halmashauri itatenga Shilingi milioni 400, uwezo wa Halmashauri yetu bado siyo mkubwa hivyo. Aliyetangulia, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, aliahidi kuleta Shilingi milioni 300. Ni lini fedha hizo zitakuja Magulilwa ili tukamilishe hiki kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jackson Gideon Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue nafasi hii kuwapongeza wananchi wa Kata ya Mgama kwa kutoa nguvu zao kujenga kituo cha afya na kujenga msingi kwa ajili ya wodi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumemwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Vijijini, afanye tathmini ya gharama zinazohitajika kwa ajili ya ukamilishaji wa wodi hiyo ili Serikali ione namna ya kutafuta fedha kwa kushirikiana Halmashauri kwa maana ya mapato ya ndani kukamilisha ujenzi wa wodi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, ni kweli kwamba Mheshimiwa Waziri wa Nchi, aliahidi kupeleka Shilingi milioni 300 fedha ya Serikali kwa ajili ya kujenga kituo cha afya pale Magulilwa. Katika jibu la msingi tumetenga Shilingi milioni 400 kupitia mapato ambayo ndiyo fedha ya Serikali hiyo hiyo kwa kwa jili ya ujenzi wa kituo cha afya hicho. Ahsante.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kule Magu Lutale, Wamanga na Igogo, kuna uhitaji mkubwa sana wa vituo vya afya: Je, Serikali ina mpango gani kuyaangalia maeneo yale ambayo yako mbali na huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniventura Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ambazo amezitaja Mheshimiwa Mbunge ikiwepo ya Mtalia na hizo nyingine mbili kwa kadri ya uhitaji wa vituo vya afya, Serikali ilishatoa maelekezo kwamba Halmashauri ziainishe kata za kimkakati kwa ajili ya kujenga vituo vya afya, kwa kuwa hatujengi kituo cha afya kila kata wala hatujengi zahanati kila Kijiji, bali tunajenga vituo vya afya kwenye kata za kimkakati ambazo zina vigezo ambavyo vinaelezea na pia zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge kwamba twende tukaainishe haya maeneo kama ni maeneo ya kimkakati na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Magu alete Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kwenda hatua inayofuata.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi, Kata ya Korongwe na Kata ya Mkwamba kuna umbali wa kutosha kufika katika hospitali ya wilaya, na hizo kata zote mbili hazina vituo vya afya: Nataka kujua mkakati wa Serikali ili kuwaokoa wanawake ambao wamekuwa wanajifungulia njiani na kupewa penalty, wanalipa Shilingi 50,000?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Nkasi ni miongoni mwa Halmashauri ambazo bado zina kata ambazo hazina vituo vya afya, na tayari Mkurugenzi alishawasilisha kata za kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kata hizi mbili ni sehemu ya kata ambazo tutakwenda kutafuta fedha, kwa kushirikiana na Halmashauri, kwa maana ya mapato ya ndani na Serikali Kuu ili kuanza ujenzi wa vituo vya afya hivi kwa awamu.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Msingi wa uanzishwaji wa maboma ya zahanati ulitokana na uliokuwa mradi wa uendelezaji wa mitaji katika Serikali za Mitaa. Hivyo katika Bunge la Kumi na Moja, lilitaka Serikali kukamilisha maboma hayo baada ya mradi huo kwisha. Je, Serikali haioni haja ya kupeleka mwongozo wa matumizi ya fedha katika fedha za kukamilisha maboma ya zahanati? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, takribani ni miaka miwili sasa Serikali imepeleka fedha 2021/2022: Je, Serikali iko tayari kufanya sensa ya kuangalia fedha zilizopelekwa kukamilisha maboma, zinaendana na maboma yaliyokamilishwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilipeleka mwongozo wa namna ambavyo fedha zinazopelekwa kwa ajili ya kukamilisha maboma ya zahanati Shilingi milioni 50 kwa kila boma zinatakiwa kutumika na kukamilisha maboma yale. Moja ya maelekezo ilikuwa ni kwamba, boma ambalo linaombewa fedha, Shilingi milioni 50 lazima liwe limefika hatua ya renter, siyo msingi au chini ya renter. Hesabu zilifanywa kwamba Shilingi milioni 50 ipelekwe kwenye jengo ambalo limefikia hatua ya renter linakamilika na kuanza kutoa huduma za afya mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali kila inapopeleka fedha, inapeleka na mwongozo, na pia tunafuatilia kuona utekelezaji wa miradi hiyo kwa mujibu wa mwongozo uliopelekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na kufanya tathmini kama fedha ambazo zilipelekwa kwa ujenzi wa maboma zimekamilisha; katika mwaka wa fedha uliopita zaidi ya maboma 555 yamelekewa Shilingi milioni 50, lakini zaidi ya asilimia 85 mpaka Juni mwaka huu yalikuwa yamekamilika, na yako hatua za mwisho za kusajiliwa. Tunaendelea kufanya tathmini kuhakikisha fedha hizo zinaleta tija kwa wananchi.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Mbugani katika Jimbo la Tabora Mjini ina uhitaji mkubwa sana wa zahanati. Sijui Serikali ina mpango gani wa kuisaidia Kata hiyo ya Mbugani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata hii ya Mbugani ambayo ina uhitaji wa zahanati, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, kufanya tathmini kujiridhisha na vigezo vya kujenga zahanati ya kimkakati na baada ya hapo kuona mapato ya ndani, na pia kuleta maombi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kwa kutumia mapato ya ndani na Serikali kuu tuone uwezekano wa kutekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Nilikuwa na maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaishukuru Serikali kwamba imetujengea vituo vitatu vya afya kwa mwaka uliopita, ambapo kuna Kituo cha Ndanto, Kituo cha Kiimo pamoja na Kituo cha Ikinjola ambavyo viko mwishoni kabisa kukamilika na watumishi wameshapelekwa; je, ni lini vifaa tiba katika vituo hivyo vya afya vitapelekwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kwenye Kituo cha Afya cha Masukuru, jengo la X-Ra, liko tayari, pia na jengo la mortuary liko tayari, lakini kwa bahati mbaya sana x-ray hatuna na mtumishi wa mortuary pale katika Kituo cha Afya Masukuru hakuna. Ni lini x-ray pamoja na mtumishi wa mortuary katika Kituo cha Afya cha Masukuru watapelekwa? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipokee shukrani za Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali hii Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kujenga Vituo vya Afya vitatu ndani ya mwaka mmoja. Nimhakikishie kwamba mipango ya ujenzi wa Vituo vya Afya inakwenda sambamba na mipango ya ununuzi wa vifaa tiba. Katika bajeti ya mwaka huu Serikali imetenga jumla shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya vifaa tiba kwenye vituo vya afya 530. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pia tutatoa kipaumbele kwenye vituo vya afya ambavyo vimekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na ukosefu wa mashine ya x-ray na mtumishi wa mortuary, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kununua vifaa tiba hivi kwa awamu. Kwa hiyo, mara pale tutakaponunua x-ray za kutosha basi kituo hiki cha afya pia kitatazamwa pamoja na kupelekewa mtumishi wa mortuary, ahsante. (Makofi)
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Katika Kata ya Wazo, Jimbo la Kawe tayari zahanati imekamilika, lakini hakuna Jengo la Mama na Mtoto. Ni lini Serikali itajenga jengo hilo ili kunusuru uhai wa akinamama hao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba katika Kata ya Wazo zahanati imekwishajengwa lakini hakuna Jengo la Mama na Mtoto, lakini nafahamu Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni haiwezi kushindwa kujenga Jengo la Mama na Mtoto. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kutenga fedha kwa ajili ya kujenga Jengo la Mama na Mtoto katika zahanati hii kwenye Kata ya Wazo.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Naibu Spikaa, nakushukuru sana. Napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge imeshafanya tathmini kuhusu mahitaji ya maeneo ya kujenga vituo vya afya ambako kuna watu wengi na ni mbali. Kituo cha Afya katika eneo la Kata za Igigwa, Kiloleli, Ipole na Usunga. Je, ni lini Serikali itatusaidia kujenga vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda, Mbunge wa Jimbo la Sikonge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka utaratibu wa kuainisha maeneo yote ambayo ni ya kimkakati kwa ajili ya kujenga Vituo vya Afya kwenye Kata na Tarafa za kimkakati na nakumbuka Mheshimiwa Mbunge alikwisha wasilisha kata hizo kwa ajili ya kujenga hivyo vituo vya afya na sisi tunafanya tathmini kujiridhisha tu na vigezo vile, lakini nimhakikishie kwamba tunafahamu Halmashauri ya Wilaya ya Sikonge ni moja ya halmashauri kubwa na ina umbali mkubwa kati ya kata na kata, hivyo tutaweka kipaumbele katika ujenzi wa vituo hivyo vya afya.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, naomba kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Halmashauri ya Wilaya ya Geita ni moja ya Halmashauri mpya ambazo zilianzishwa miaka michache iliyopita. Ambazo watumishi wake wengi bado wanaishi kwenye Halmashauri za zamani. Kwa kuwa, Serikali kupitia Wizara ya Ardhi na NHC, imekuwa ikijenga nyumba na kukopesha watumishi na Halmashauri hiyo ina viwanja tayari vimepimwa. Ni kwa nini TAMISEMI, wasiingie mkataba na Wizara ya Ardhi, kujenga nyumba na kuirahisishia Halmashauri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Miji mingi Tanzania imekuwa ikikua lakini kwa ujenzi holela. Kwa nini Serikali kwa sababu ni sharti moja la Miji hiyo kupanda hadhi na kuwa Manispaa au Miji mikubwa isiingie utaratibu na Wizara ya Ardhi kuipima Miji yote ili kuzuia ujenzi holela ambao unaendelea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, Mheshimiwa Constantine Kanyasu, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwanza kuhusu suala la Ofisi ya Rais – TAMISEMI, kuingia makubaliana na Wizara ya Ujenzi kwa ajili ya kuitumia NHC kujenga nyumba za watumishi, Serikali imekuwa ikifanya hivyo katika Halmashauri mbalimbali. NHC wamejenga nyumba na watumishi wameuziwa au wanapangishwa na wanaendelea huduma katika maeneo hayo. Kwa hiyo, tumepokea wazo la Mheshimiwa Kanyasu tutafanya utaratibu huo ili kuona uwezekano wa kujenga nyumba hizo katika Halmashauri ya Geita Vijijini lakini pia Geita Mjini baada ya kuongea na Wizara ya Ujenzi.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kuhusiana na upimaji wa Miji, Serikali ilishaweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba Mamlaka za Serikali za Mitaa zinatekeleza jukumu lao la kupima ardhi katika maeneo yao. Kwa hiyo, suala hili ni suala la msingi na jukumu la msingi la Halmashauri kazi zinaendelea, ni kweli kwamba kasi ya upimaji imekuwa ndogo na ujenzi holela umeendelea kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue fursa hii kuwaelekeza Wakurugenzi wa Halmashauri zote kote nchini, kuhakikisha wanatekeleza wajibu wao wa kupima maeneo ya ardhi katika Miji ili kuzuia ujenzi holela. (Makofi)
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu imekamilisha jengo la utawala na wamehamia katika makao mapya yaliyoko Dongobeshi, lakini kuna changamoto kubwa ya nyumba za watumishi.

Je, Serikali itawejengea lini nyumba za watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba jengo la Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu limekamilika lakini kuna changamoto ya nyumba za watumishi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeweka mpango baada ya kukamilisha jengo la watumishi sasa tutakwenda kufanya utaratibu wa kujenga nyumba za watumishi ili watumishi waishi karibu na Makao Makuu ya Halmashauri na kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Halmashauri ya Mji ya Bunda ni mpya tayari imejenga jengo la ofisi ya Halmashauri, lakini kuna changamoto kubwa sana ya nyumba za watumishi wakiwemo Walimu, Madaktari na watumishi wa halmashauri. Ni lini sasa Serikali itajenga na hasa ukisema utegemee Halmashauri ya Bunda mapato yake ni madogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Halmashauri ya Mji wa Bunda, imejengewa jengo la halmashauri kwa maana ya jengo la utawala, lakini changamoto ya nyumba za watumishi ipo na Serikali inatambua changamoto hiyo. Nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Bunge Mjini kwamba wewe pamoja na Mheshimiwa Mbunge Maboto mnashirikiana vizuri kuhakikisha nyumba za watumishi zinajengwa pale na Serikali itaendelea kufanya utaratibu kuona uwezekano wa kujenga nyumba za watumishi pale.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa kuna upungufu mkubwa wa nyumba za walimu katika shule za msingi na sekondari Mkoa wa Simiyu.

Je, ni lini Serikali itajenga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba Mkoa wa Simiyu lakini pia Mikoa yote kote nchini bado kuna changamoto ya upungufu wa nyumba za watumishi wa sekta ya afya, sekta ya elimu pia sekta na idara nyingine. Mpango wa Serikali tumeendelea kujenga nyumba za watumishi lakini safari ni hatua tunakwenda kwa awamu. Tumeendelea kujenga, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kutumia mapato ya ndani ya Halmashauri hizo, Serikali imeelekeza kuhakikisha wanaanza kutenga fedha kwa ajili ya kujenga nyumba hizo, pia Serikali Kuu itaendelea kujenga kwa awamu. Ahsante. (Makofi)
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru Mbunge wa Viti Maalum, Mkoa wa Morogoro.

Je, ni lini Serikali itahakikisha dawa zote zinazohitajika kwenye wodi za kinamama na vipimo vyote zinapatikana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika Kituo cha Afya cha Mkoani Ruvuma, Wilaya ya Songea, Kata ya Ruvuma, kumekuwa na tatizo la Madaktari na Matabibu ambao ni wachache sana hawakidhi kutoa huduma ya afya ipasavyo.

Je, ni lini Serikali itaongeza Madaktari na Matabibu kwenye kituo cha afya hiki ili huduma sahihi ziendelee kutolewa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, tumeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa lakini pia vitendanishi na vifaa tiba katika vituo vyetu. Katika kipindi cha mwaka huu fedha nyingi zimetengwa kwa ajili ya kununua vifaa tiba, Bilioni 69.95 kwa ajili ya kununua vifaatiba katika Vituo vya Afya 530 nchini kote.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha uliopita, bajeti ya dawa imeongezeka na mwaka huu wa fedha bajeti ya dawa imeongezeka. Kwa hiyo, nimhakiksishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imedhamiria kuhakikisha inaondoa changamoto ya upungufu wa baadhi ya dawa kwenye Wodi za Wazazi lakini kwenye vituo kwa ujumla lakini kuboresha huduma za vipimo vya maabara.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na Kituo cha Afya katika Kata ya Ruvuma juu ya uchache wa Madaktari na Matabibu, Serikali imeendelea kuajiri watumishi, mtakumbuka mwisho mwa mwaka uliopita watumishi wa afya zaidi ya 7,000 wameajiriwa na kupelekwa nchini kote, zoezi hili ni endelevu tutaendelea kuajiri kwa kadri ya upatikanaji wa fedha ili watumishi hawa watoe huduma bora za afya katika vituo.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itaanzisha huduma za upasuaji katika Kituo cha Afya cha Mafiga, Mkoani Morogoro Manispaa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dokta Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya vikijengwa vinajengwa na majengo ya upasuaji na dhamira ya Serikali ni mara tu majengo ya upasuaji yakikamilika huduma za upasuaji zianze. Kwa hiyo, kama Kituo hiki cha Afya, Mafiga, jengo la upasuaji limekwishakamilika, naelekeza Halmashauri ya Manispaa ya Morogoro waanze huduma za upasuaji haraka iwezekanavyo, lakini kama kituo hakijakamilika wakamilishe na baada ya hapo wasajili ili huduma za upasuaji ziweze kuanza. Ahsante. (Makofi)
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itarekebisha au kupunguza bei ya huduma ya upasuaji hasa ya uzazi katika hospitali za rufaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha inatoa huduma ambazo zinaendana na gharama kwa maana ya kupunguza gharama za matibabu na hasa eneo la upasuaji. Katika hospitali za Rufaa za Mikoa, bado gharama za upasuaji ni changamoto na tumekubaliana na Wizara ya Afya, pia katika maeneo ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Vituo vya Afya na hospitali za Halmashauri, bado gharama za upasuaji ni kubwa. Kwa hiyo, tunapitia lakini baada ya muda tutatoa gharama ambazo zitakuwa zinafikika kirahisi kwa wananchi wetu. Ahsante.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Napenda kuiuliza Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa jengo la x-ray katika Kituo cha Afya Inyecha, kwa sababu Serikali imeshaleta mashine ya x-ray na wananchi kwa nguvu zao wamejenga hadi hatua za boma.

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha jengo hilo la x-ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abdallah Chikota, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imekwishapeleka mashine ya x-ray katika Kituo hiki cha Afya cha Inyecha, lakini jengo lile halijakamilika tumekubaliana na Halmashauri, kwanza watenge fedha kwa ajili ya kukamilisha jengo hilo, pia Serikali itaona namna ya kuongeza nguvu ili kukamilisha jengo hilo na kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Je, ni lini Serikali italeta mashine ya ultra sound kwa ajili ya wanawake wajawazito katika Hospitali ya Rufaa ya Ligula? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anastazia Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mtwara, maarufu kwa jina la Ligula, iko chini ya Wizara ya Afya nasi kama Serikali tunachukua hoja hiyo kuona uwezekano wa kupeleka mashine ya ultra sound mapema iwezekanavyo. Ahsante.
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana Mheshimiwa Spika, nauliza ni lini Zahanati ya Mdunduwaro – Songea Vijijini itamalizika ili wananchi wale wapate huduma, toka 2014?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Thea Medard Ntara, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ntara, amekuwa akifuatilia sana suala la Zahanati ya Mdunduwaro nami nimekwisha wasiliana na Watendaji mara kadhaa tukiwa nae na ujenzi unaendelea vizuri hatua za ukamlisha. Tulishakubaliana, ifikapo Septemba, mwisho mwaka huu Zahanati ya Mdunduwaro itaanza kutoa huduma. Kwa hiyo, nichukue fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Songea, kuhakikisha kwamba zahanati hii inakamilika mwisho mwa mwezi Septemba, ianze kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. JASEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Pamoja na majibu yake nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Kagera/Nkanda iko kilomita 70 kutoka Makao Makuu ya Wilaya. Kutoka Kagera/Nkanda mpaka Mgonde mara nyingi hutokea uhalifu wa utekaji wa magari, ikitokea dharura usiku wanawake wanashindwa kufikishwa katika hospitali ya Wilaya kutokana na kuogopa kutekwa magari usiku.

Je, ni lini sasa Serikali itapeleka gari la kubebea wagonjwa katika Kata ya Kagera/Nkanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kwamba Kata hii ya Kagera Nkanda iko mbali sana kutoka Makao Makuu na ndiyo maana katika mwaka ujao wa fedha Serikali itatenga Milioni 500 kuhakikisha tunajenga kituo cha afya katika Kata hii na kuondolea wananchi changamoto ya kusafiri umbali mrefu kwenda kupata huduma za afya katika hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba katika mwaka huu wa fedha, Serikali itapeleka magari ya wagonjwa, Halmashauri hii pia itapata gari moja la wagonjwa. Kwa hiyo, sasa Halmashauri inaweza kuona namna ya kulipeleka katika eneo hili ili litoe huduma bora kwa wananchi wa Kata hiyo. Ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kata ya Kalembo, Isongole pamoja na Malangali katika Wilaya ya Ileje ni miongoni mwa Kata ambazo hazina kituo cha afya. Naomba kufahamu, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata hizo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Shonza, amekuwa mara kwa mara akiulizia kuhusiana na Kata hizi na amekuwa akiwasemea kwa dhati wananchi wa Mkoa wa Songwe. Nimhakikishie kwamba Serikali itaendelea kuhakikisha inakwenda kwa awamu na kimkakati kujenga vituo vya afya katika Kata ambazo amezitaja. Ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Kizazi ambacho kimejengwa kwa nguvu za wananchi katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Florence Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wananchi wa Kata aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge wametoa nguvu zao, wameanza ujenzi wa kituo cha Afya na Mheshimiwa Mbunge amekuwa akifuatilia. Tumekubaliana kwamba tukipata fedha tutakwenda kuchangia nguvu za wananchi pale, kituo cha afya kikamilike tuanze kutoa huduma za afya. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunakwenda kutafuta fedha kwa ajili ya kazi hiyo. Ahsante.(Makofi)
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii, Vituo Vya Afya cha Chihangu pamoja na Mkwedu muda mrefu havina wodi za kulaza wagonjwa.

Je, ni lini Serikali itaenda kujenga wodi katika Vituo hiyo vya Afya vilivyoko Jimbo la Newala Vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Mtanda Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyetu vya afya vingi havina wodi za wazazi pamoja pia na wodi za wagonjwa wengine, kama vituo hivi ambavyo Mheshimiwa Maimuna Mtanda amevitaja. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tuna mpango wa kuhakikisha vituo vyote ambavyo havina majengo toshelezi tunakwenda kujenga majengo hayo kwa awamu ili yaweze kutoa huduma bora za afya kwa wananchi.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa hii nafasi.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Msiha na Kata ya Hiyanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga Mbunge wa Jimbo la Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshatoa maelekezo kwa Halmashauri zetu zote kuweka vipaumbele vyao vya ujenzi wa vituo vya afya katika tarafa na kata za kimkakati. Kwa hivyo kama hizi ni kata za kimkakati, nimhakikishie Mheshimiwa Hasunga, kwamba Serikali kupitia mapato ya ndani lakini kupitia fedha ya Serikali Kuu tutaendelea kuweka hatua za ujenzi ili vituo viweze kukamilika. Ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa tulishasema tumalize vituo vya afya kwenye tarafa ambazo hazina: -

Je, ni lini Serikali itajenga Vituo kwa Tarafa za Makame, Dosudosi na Kibaya ambazo bado hazina? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Wakili Olelekaita Mbunge wa Jimbo la Kiteto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli, Jimbo la Kiteto lina Tarafa ambazo bado hazina Vituo Vya Afya, na Mheshimiwa Mbunge amekuwa mara kwa mara akifuatilia hili. Nimhakikishie, kwamba mpango wa Serikali ni kujenga vituo vya afya vya kimkakati katika tarafa ambazo hazina vituo vya afya, na tutakwenda pia kutoa kipaumbele katika Tarafa za Jimbo la Kiteto ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, je lini Serikali itajenga Vituo Vya Afya katika Kata za Nyamigogo, Kabindi, Kaniha, na Nyatakala Wilayani Biharamulo? Kwa sababu tuna uhitaji mkubwa wa Vituo Vya Afya katika maeneo hayo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eng. Ezra Chiwelesa Mbunge wa Jimbo la Biharamulo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata alizozitaja Mheshimiwa Mbunge na uhitaji wa vituo vya afya tutakwenda kufanya tathmini na kuona uwezekano wa mapato ya ndani kujenga vituo hivyo, lakini pia kutafuta fedha Serikali Kuu kwa ajili ya kujenga vituo hivyo kama vitakidhi vigezo vile vya kujenga vituo vya afya katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Naomba kujua, je, gari la wagonjwa lililoahidiwa kwenye Kituo Cha Afya Mgeta litaenda lini kwenye kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Boniphace Mwita Getere Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata aliyoitaja na uhitaji wa kituo cha afya hicho tutakwenda kuona uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho kama kitakidhi vigezo tulivyoweka kwa ajili ya vituo vya afya vya Kimkakati ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je lini Serikali itajenga Vituo Vya Afya katika Kata za Igundu, Muhura na Kitengule katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kajege Mbunge Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata alizozitaja Mheshimiwa Mbunge zinahitaji vituo vya afya, na amekwisha leta kama vipaumbele vya jimbo lake. Nimhakikishie, kwamba tumekubaliana na halmashauri, kwamba kwanza waanze kutenga fedha kwa awamu kupitia asilimia arobaini ya mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vya afya hivyo; lakini pia Serikali itakwenda kuunga mkono nguvu hizo kwa ajili ya kukamilisha vituo vya afya katika maeneo hayo. Ahsante sana.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, kwanza kutokana na majibu haya naomba nimpongeze Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Hanifa Suleman Hamza ambapo mwaka jana yeye amefanikisha kupeleka mikopo ya asilimia mia moja ya shilingi bilioni 3.1 kwa watu wa Kinondoni, nimpongeze kwa hilo.

Mheshimiwa Spika, swali langu, kwa kuwa marejesho yanaonekana hayakuwa asilimia mia moja kuna asilimia 31 ya fedha za mikopo hazijarejeshwa. Je, Serikali ipo tayari kufanya performance audit ili kuweza kujua kama fedha hizi kweli ziliwafikia walengwa na sababu ya kutokurudishwa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Serikali iko tayari kufanya utafiti kujua kwamba fedha hizi zinapopelekwa kwa walengwa hakika zinawafikia na zinabadilisha Maisha yao kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika kipindi hiki cha miaka mitano marejesho yalikuwa asilimia 69.32 na Serikali ilifanya performance audit kwa kuhakikisha kwamba tunaita halmashauri zote 184 na kuona mtiririko wa mikopo kwa miaka yote mitano.

Mheshimiwa Spika, maelekezo tuliyoyatoa Serikali ni kuhakikisha tunabainisha vikundi vyote ambavyo vilikopeshwa na vilikuwa havikurejesha marejesho hayo na virejeshe marejesho hayo. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari marejesho yanakwenda vizuri, kwa vikundi vyote ambavyo vilikopa na vilikuwa havijarejesha.

Mheshimiwa Spika, pili, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwanza tumeanzisha mfumo wa kielektroniki wa kikopeshaji wa mikopo wa asilimia kumi, na halmashauri zote zimelekezwa kuingiza vikundi vyote vilivyokopeshwa na ambavyo havijarejesha kwenye mfumo wa kielektroniki ambao tutaufutilia kila siku na kuona kila hatua ya marejesho ya fedha hizo. Kwa hiyo, mpango huu wa asilimia kumi umeboreshwa kwa kiasi kikubwa na marejesho yanakwenda vizuri. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Ni kweli majengo yameshaanza kujengwa katika kituo cha Itobo pamoja na kuendeleza; Serikali imekuwa ikipeleka fedha na kujenga majengo nusu baadhi ya vituo, kikiwemo Kituo cha Igalula, jengo la OPD halijajengwa, Kituo cha Lutete majengo hayajakamilika: -

Je, nini mikakati ya Serikali kupeleka fedha kumalizia vituo vya afya vyote ili wananchi waendelee kupata huduma? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant Protas, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikijenga vituo vya afya kwa awamu kwa kupeleka fedha awamu ya kwanza kujenga majengo ya awali na awamu ya pili kumalizia majengo yaliyobaki.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge, kuna baadhi ya vituo vya afya vimepata awamu ya kwanza Shilingi milioni 250, vitapelekewa awamu ya pili Shilingi milioni 250 kutimiza Shilingi milioni 500. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vituo vya afya ambavyo bado havijakamilishwa, fedha itapelekwa awamu ya pili ili kukamilisha majengo yale na vituo vianze kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante sana.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru wa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wakati wa ziara ya Mheshimiwa Waziri Mkuu pale Kijiji cha Chomachankola, Tarafa ya Choma, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliahidi kutupatia fedha kuongeza kwenye Kituo cha Afya cha Choma: -

Je, ni lini sasa Wizara italeta fedha kwa sababu ahadi hii imetolewa toka 2018? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Seif Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali iliahidi kupeleka fedha kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Choma, Kijiji cha Chomachankola katika Jimbo la Manonga na ni kweli kwamba Mheshimiwa Mbunge amefuatilia kwa karibu sana, na mwaka wa fedha uliopita tulikosa kifungu cha kupelekea fedha ile, lakini nimeongea naye na tumekubaliana katika mwaka wa fedha huu tutahakikisha fedha inapelekwa ili kitu cha afya kianze kujengwa. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Mwaka 2008 Serikali ilianza ujenzi wa jengo la mama na mtoto kwenye zahanati ya Kijiji cha Msada, Kata ya Msada, lakini mpaka leo ni miaka 14 lipo kwenye renter. Naomba kujua ni lini sasa Serikali itatoa fedha za kumalizia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali iliweka utaratibu wa kutumia fedha kutoka Serikali Kuu na pia kutumia fedha kutoka mapato ya ndani halmashauri kukamilisha baadhi ya majengo na hususan majengo katika ngazi ya zahanati. Kwa hiyo, naomba nichukue fursa hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, kuhakikisha wanatenga fedha katika asilimia 40 ya miradi ya maendeleo kukamilisha jengo la mama na mtoto katika zahanati ambayo Mheshimiwa Mbunge ametaja. Ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi. Je, ni lini Serikali itaboresha kituo cha afya cha Ndalambo ikiwa ni sambamba na kuongeza majengo? Kituo hiki kinahudumia kata zaidi ya tano zilizopo kwenye Tarafa ya Ndalambo. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Jimbo la Momba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya vituo vya afya ambavyo ujenzi wake ulianza, lakini haujakamilika na inaweka mpango wa kukamilisha vituo vya afya vile havijakamilika ili viweze kutoa huduma za afya kwa wananchi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kuwa kituo kile kilishaanza ujenzi na hakijakamilika, tutakwenda kukamilisha kituo hicho.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii pia kutoa taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba mpango na dhamira ya Serikali ni kukamilisha kwanza vituo vya afya ambavyo vilianza ujenzi na havijakamilika ili vipate vifaa tiba na kuanza kutoa huduma za afya kabla ya kuendelea kujenga vituo vingine vipya. Vile vile tutaendelea kujenga zahanati za kimkakati isipokuwa vituo vya afya vipya mpaka pale tutakapokuwa tumekamilisha ujenzi wa vituo vya vya afya ambavyo tayari vimeshaanza. Ahsante sana.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa kuwa Kata ya Mlowa, Kijiji cha Mkolango, wananchi wa Mkolango wamejenga zahanati pamoja na Diwani na Mbunge; na Rais alipokuja tulimweleza jambo hili na aliahidi kwamba sasa atakwenda kumalizia kwa sababu imekwisha, wameshaezeka na kila kitu; na Naibu Waziri na Waziri walikuwepo na ndiyo mlisikia: Sasa je, ni lini mtatuletea fedha ili wananchi wa Mkolango muweze kuwaunga mkono zahanati hii imaliziwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kuwapongeza wananchi wa Kata ya Mlowa, Kijiji hiki cha Mukolango kwa kutoa nguvu zao kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge kuanza ujenzi wa zahanati. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, katika bajeti ya Serikali ya mwaka huu wa fedha, fedha zimetengwa kwa ajili ya kukamilisha maboma ya zahanati na tutatoa kipaumbele katika zahanati hii ambayo Mheshimiwa Mbunge amesema. Ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kituo cha Afya cha Changuge, Tarafa ya Gelango, Wilaya ya Rorya ni moja ya kituo ambacho kimejengwa muda mrefu sana na kwa sasa majengo yake yamechakaa na hata yaliyopo hayatoshelezi kulingana na mahitaji ya tarafa na kata ile. Nataka nijue mpango wa Serikali sasa kuboresha vituo vya afya vile vya zamani ili angalau viendane sasa na kasi na uhitaji wa wananchi wa sasa. Nini mpango wa Serikali katika kuboresha vituo vya afya vya zamani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jafari Chege, Mbunge wa Jimbo la Rorya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika maeneo mbalimbali kote nchini kuna baadhi ya vituo vya afya na hospitali za halmashauri ambazo ni chakavu, na Serikali imeweka kanzidata kwa kutambua vituo vya afya chakavu na itaendelea kutenga fedha kwa awamu kwa ajili ya ukarabati wa vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba tuichukue hii hoja ya Mheshimiwa Mbunge, tufanye tathmini ya kituo hicho cha afya na kuona uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya matengenezo. Ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naishukuru Serikali kwa majibu mazuri. Pamoja na hayo niombe kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; katika bilioni 2.36 ambazo zilipelekwa Hospitali ya Wilaya, zilichukuliwa milioni 400 ambazo zilikuwa kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Iramba katika Jimbo langu la Serengeti na hali ya afya kule ni mbaya, ni kituo cha muda mrefu kimechakaa na kinahudumia watu wengi. Je, ni lini Serikali itapeleka tena hizo fedha milioni 400?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hospitali ya Nyerere DDH inahudumia zaidi ya wakazi 100,000 katika Jimbo langu na idadi ya watumishi Saba iliyopelekwa bado kuna upungufu wa Madaktari 22, Wauguzi Wasaidizi 28 na Wauguzi wa kawaida 37.

Je, ni lini Serikali itatusaidia kuhakikisha tuna Madaktari wa kutosha na Wauguzi wengine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali ilipeleka Shilingi Bilioni 2.36 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Serengeti, kati ya fedha hizo, Shilingi Milioni 400 ilipelekwa kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Iramba. Sasa kwa sababu Halmashauri walitumia fedha ile kujenga majengo ya hospitali ya Wilaya, kwanza naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Serengeti kuhakikisha wanazingatia maelekezo ya Serikali. Fedha inapopelekwa kwa ajili ya kujenga vituo vya afya ijenge vituo vya afya kama ni zahanati ijenge zahanati, kama ni hospitali ijenge hospitali badala ya kuhamisha matumizi bila kibali maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, natoa maelekezo katika mapato yao ndani watenge kwa awamu Shilingi Milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Iramba.

Mheshimiwa Spika, kuhusina na Hospitali ya Nyerere DDH, ni kweli kwamba ina upungufu wa watumishi lakini Serikali imeendelea kupeleka watumishi, katika mwaka huu wafedha imetengewa ajira Saba kwa ajili ya kuonesha kwamba tunaendelea kupunguza upungufu wa watumishi katika hospitali hiyo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba kuuliza Serikali ni lini italeta fedha za awamu ya pili kuwezesha ujenzi wa hospitali ya Wilaya ya Ngara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndaisamba, Mbunge wa Jimbo la Ngara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hospitali ya Wilaya ya Ngara ilipelekewa shilingi Milioni 500 mwaka wa fedha uliopita na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunajenga hospitali zetu hizi kwa awamu, sasa tunakwenda awamu ya pili ambapo katika mwaka wa fedha huu hospitali hii pia imetengewa Shilingi Milioni 500 na zitakwenda wakati wowote ndani ya mwaka huu wa fedha.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka vifaa tiba ikiwemo mtambo wa kuzalisha oxygen katika hospitali ya Wilaya Meatu katika jengo la mahututi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka huu wa fedha imetenga Shilingi Bilioni 69.95 kwa ajili ya kununua vifaa tiba na kuvipeleka katika vituo na hospitali zetu kote nchini. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwanza bajeti ya vifaatiba katika hospitali ya Wilaya ya Meatu tayari ipo, lakini tutakwenda kufanya tathmini kuona uwezekano wa kuwa na mtambo wa kuzalisha oxygen kulingana na mahitaji ili tuweze kuona namna ya kutekeleza wazo hilo.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hospitali ya DDH ya Ilula, bado inategemewa sana wananchi wa Tarafa ya Mazombe na Tarafa ya Mahenge. Je, Serikali ina mpango gani wa kuendelea kuipelekea fedha hospitali ili iweze kutoa huduma bora kama ilivyokuwa ikitoa mwanzo ilivyokuwa DDH kabla ya kujengwa hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justine Nyamoga, Mbunge wa Jimbo la Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuhakikisha inawezesha hospitali zetu hizi za DDH kuendelea kutoa huduma kwa wananchi katika maeneo hayo. Kwanza kwa kuhakikisha kwamba fedha za mfuko wa pamoja health center basket fund zinaendelea kupelekwa, Hospitali hii ni moja ya hospitali zinazoendelea kupewa fedha hizo ili kuziwezesha kujiendesha na kutoa huduma bora, lakini pia kuangalia uwezekano wa kuendelea kuwapatia watumishi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuiunga mkono hospitali hii ili iendelee kutoa huduma kwa wananchi wa Mazombe na Tarafa zingine za karibu.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza, pamoja na majibu mazuri ya Serikali swali lina maelezo madogo.

Kwa kuwa, fedha nyingi zinapelekwa za maendeleo katika Halmashauri zetu nchini zikiwepo za afya, barabara, maji, elimu. Na kwa kuwa hivi karibuni Rais wetu mpendwa mama Samia Suluhu Hassan ametupatia fedha nyingi za kujenga madarasa katika sekondari zetu Mabilioni kwa Mabilioni. Sasa Madiwani hawa hawasimamii kwenye force account hawamo, na hawa ndiyo wanaowaeleza wananchi tumepata fedha kiasi gani.

Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka Madiwani hawa wawemo ili kusudi maana ndiyo wanaowaambia wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa vilevile kama nilivyosema ndiyo wanaosimamia na Serikali posho za mwezi tulizungumza kwenye bajeti hapa tunaomba waongezewe. Je, Madiwani wote nchini, bajeti ya 2023/2024 Serikali imejipangaje kuwaongezea posho za mwezi madiwani hawa nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hospitali ya Awamu ya Sita, chini ya Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan imeleta fedha nyingi sana katika Halmashauri zetu katika utekelezaji wa miradi mbalimbali. Lakini nimhakikishie kwamba kwa mfumo wa force account, kwa kuwa Waheshimiwa Madiwani ni viongozi wasimamizi wa miradi hiyo, mwongozo wa haukuwaweka Madiwani kuwa sehemu ya Kamati zile kwa sababu wanahitaji kuhoji zile Kamati. Kwa hiyo, kama Diwani atakuwa sehemu ya Kamati ile atashindwa kujihoji mwenyewe lakini atashindwa kusimamia wananchi katika maeneo yale katika kutekeleza miradi ile.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ninamuombe Mheshimiwa Mbunge aamini kwamba dhamira ya Serikali ni nzuri kwamba Waheshimiwa Madiwani wabaki na nguvu zao za kusimamia na kuhoji Kamati ili miradi iweze kutekelezwa kwa ubora zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na posho za Waheshimiwa Madiwani, kwanza niwahakikishie kwamba Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan anathamini na anajali sana kazi kubwa inayofanywa na Waheshimiwa Madiwani na ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha amechukua jukumu la Serikali Kuu kulipa posho za Madiwani kama Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba Serikali inafanya tathmini ya kuona uwezekano na uwezo wa Serikali kuongeza posho hizo ili muda ukifika posho hizo ziongezeke kwa ajili ya Waheshimiwa Madiwani. Ahsante. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri nina mashaka nayo, kwa sababu wako wamachinga wengi Jiji la Arusha ambao wamekosa maeneo ya kufanyia baishara.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia taarifa ya Mheshimiwa Naibu Waziri ametuambia kwamba kwa sasa wao wamewatambua wamachinga 5,426 na kati ya hao wametoa vitambulisho kwa wamachinga 1187, je ni kwa nini wamachinga waliobaki mpaka sasa hivi hawajapata vitambulisho na wanaendelea kuchajiwa ushuru na Halmashauri ya Jiji la Arusha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa mgambo ambao wanatumwa na Halmashauri ya Jiji la Arusha kupitia Mkurugenzi wa Jiji wamekuwa wanapora vitu vya watu vinakwenda kuwekwa kule depo vinaoza pia wanachukua fedha za watu nje ya utaratibu kiasi cha kuleta manyanyaso na kufanya hali ya kisiasa...

SPIKA: Mheshimiwa Gambo sasa hapo unachangia, Mheshimiwa Gambo ulishauliza maswali.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taarifa hizi zimetoka ndani ya Halmashauri ya Jiji la Arusha kwa watendaji wa Serikali ambao wamejiridhisha idadi ya wamachinga walioko pale na idadi ya wamachinga ambao wamepewa vitambulisho. Pamoja na kwamba Serikali na Jiji la Arusha lilikuwa katika utaratibu wa kuwapanga wamachinga lakini utaratibuwa kutoa vitambulisho ulikuwa unaendelea sambamba na kuwapanga wamachinga; kwa hiyo nikutoe shaka katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kwa nini baadhi ya hawa wamachinga hawajapata vitambulisho; suala hili ni suala la kutoa elimu, kuhamasisha wale wamachinga wenye sifa waweze kutoa kwa hiari yao ili waweze kupata vitambulisho vile na kazi hii inaendelea kuelimisha ili hawa waliobaki nao wapate vitambulisho.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mgambo kuvamia na kupokea fedha na kumwaga bidhaa za wananchi, Serikali ilishatoa tamko, kwamba katika shughuli za kuwapanga wamachinga nchini kote mgambo hawahusiki na hawatakiwa kuhusika kuleta bugudha yoyote kwa wafanyabiashara. Kwa hiyo nitoe maelekezo kwa Jiji la Arusha kusimamia maelekezo ya Serikali ili wafanyabiashara hawa wasibughudhiwe na mgambo sehemu yoyote. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante, na ninamshukuru Mhehsimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri naomba niulize maswali madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; ni lini Serikali itapeleka magari ya wagonjwa kwa Hospitali ya Ilongelo na Hospitali ya Wilaya ya Manyoni iliyopo Singida?

Mheshimiwa Spika, swali la pili vituo vya afya vya Ngome na Ipogolo vimekuwa vikitumia magari ya abiria katika kusafirisha wajawazito kwenda kujifungu. Ni lini sasa Serikali itaona umuhimu pia wa kutupatia magari katika hospitali yetu ya Wilaya ya Iringa Manispaa na katika vituo hivyo vya Afya vya Iringa Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba Serikali itanunua magari ya wagonjwa 195 kwa ajili ya Halmashauri zetu zote 184 nchini kote. Kwa hivyo Kituo cha Afya na Hospitali ya Ilongelo na Manyoni zitanufaika kwa magari hayo lakini bado tutaendelea kutenga fedha kwa awamu ili vituo vingine vyote vipate magari ya wagonjwa, kwa maana ya kuboresha huduma za rufaa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Ngumi, Ipogolo na Hospitali ya Manispaa ya Iringa ni kweli ina changamoto ya gari la wagonjwa; na Manispaa ya Iringa nayo itanufaika na magari haya. Kwa hiyo changamoto hiyo kwa sehemu itakuwa imetatuliwa, lakini tutaendelea kutafuta magari zaidi.

Mheshimiwa Spika, tarehe 06 juzi Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan amezindua mpango mkakati wa M-mama ambao utawezesha rufaa za dharura katika mikoa 12 kwa kushirikisha wadau, wakiwemo Vodacom. Kwa hiyo pamoja na jitihada za Serikali lakini bado jitihada za private sector kama Vodacom tutakwenda kuondoa kabisa changamoto ya rufaa kwa wagonjwa wetu, ahsante sana.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, asante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali la nyongeza, nikiwa na hakika kabisa kwenye magari na Wilaya ya Hai itapata.

Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza ni lini Serikali sasa itatuletea vifaa tiba kwenye kituo chetu cha afya cha Longoi ambacho kimekamilika, ili kiweze kuanza kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali yetu imeendelea kutenga fedha za ununuzi wa vifaa tiba kwa awamu. Kwa sasa tayari imeshatenga kwa ajili ya Hospitali zile 67 za awamu ya kwanza lakini tutakwenda Hospitali zile 28 za awamu ya pili na vituo vya afya vitatengewa fedha baada ya kukamilika kwa hizi 67 na 28 kikiwemo Kituo hiki cha Afya katika Halmashauri ya Hai. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hicho ni kipaumbele cha Serikali na kadri ya upatikanaji wa fedha tutapeleka fedha na vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Hai.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, bado Hospitali ya Wilaya ya Pangani inakabiliwa na changamoto ya uchakavu wa vifaa kama vile generator, mashine ya kufulia na ambulance: Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha inaondoa changamoto hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kupitia fedha za tozo, Kata ya Madanga tumepata shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Kata ya Madanga: Je, ni upi mpango wa Serikali wa kuhakikisha inakwenda kukamilisha kituo hicho cha afya kwa haraka ili kuokoa maisha ya wananchi wa Kata ya Madanga, Kimang’a, Bushiri na Masaika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshemiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamilu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali hii ya Pangani ni chakavu, sambamba na hilo, ina vifaa tiba na vifaa kama mashine za kufulia chakavu na pia gari la wagonjwa ni chakavu sana. Naomba kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Mwantumu Zodo kwa namna ambavyo anasemea wananchi wa Mkoa wa Tanga na Watanzania kwa ujumla, vile vile kwa namna ambavyo anashirikiana kwa karibu sana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Pangani, Mheshimiwa Jumaa Aweso, ambaye naye pia amekuwa anafuatilia sana kuhusiana na ujenzi na ukarabati wa Hospitali ya Halmashauri ya Pangani.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mwaka huu wa fedha, Serikali imetenga fedha kwa ajili kununua magari 407 na kati ya hayo 195 ni magari ya wagonjwa na Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Pangani itapata gari jipya la wagonjwa na kuondoa changamoto hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la vifaa tiba Serikali imeendelea kutenga fedha na tutahakikisha tunaenda kwa awamu kuboresha vifaa tiba katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na kituo cha afya ambacho kimepata shilingi milioni 500, nimhakikishie kwamba kitakwenda kukamilishwa, kutafutiwa vifaa tiba na kuwekwa watumishi ili huduma za afya ziendelee kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kama ilivyo kwa hospitali kongwe, tuna vituo vya afya vikongwe na chakavu sana kama Kituo cha Afya cha Gungu kilichopo Korogwe. Ni lini Serikali italeta mkakati wa ukarabati na kuboresha vituo vya afya vya siku nyingi na chakavu ili kuwapa huduma wananchi wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshemiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava Mbunge wa Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba Serikali imefanya tathmini ya vituo vya afya chakavu vyote nchini kote na mpango unandaliwa kuhakikisha vinakarabatiwa na vinakuwa bora kwa ajili ya utoaji wa huduma za afya. Kwa hiyo, kituo hicho pia kitapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Magari ya vituo vya afya vya Mrijo, kwa Mtoro na Makorongo yamechakaa kabisa na hayafanyi kazi. Naomba commitment ya Serikali sasa kama tunaweza kufanyiwa ukarabati au kama tunaweza kupata magari mapya. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshemiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, nampongeza sana kwa kazi kubwa anayoifanya kwa wananchi wa Chemba. Nimhakikishie kwamba magari ya wagonjwa ambayo ni chakavu, Serikali inaweka mpango wa kutafuta magari mengine ya wagonjwa ili kuhakikishwa huduma za afya zinaenda vizuri na tutatoa kipaumbele katika vituo vya afya ambavyo Mheshimiwa Mbunge amevitaja. (Makofi)
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. La kwanza: Kwa kuwa mahitaji ya wahudumu wa afya katika Kituo cha Afya Gidas ni 52 na waliopo sasa ni watano tu: Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza wahudumu wa afya ili kuwasaidia wananchi hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa kituo cha afya kiko mbali na hospitali ya wilaya: Je, Serikali ipo tayari kupeleka gari la kubebea wagonjwa ili kuwasaidia wananchi wetu? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na upungufu wa wahudumu wa afya, Serikali inatambua upungufu wa wahudumu wa afya katika maeneo mbalimbali ya vituo vyetu vya huduma na ndio maana wiki iliyopita, Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Utumishi alitoa taarifa katika Bunge lako kwamba Serikali imeweka mpango wa kutoa vibali na kuanza kutoa ajira; na katika ajira hizo watumishi wa sekta ya afya watakuwemo. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafanya mkakati na mara watakapoajiriwa, tutahakikisha kituo hicho kinapata watumishi ili kuboresha huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na gari la wagonjwa, kama nilivyotangulia kujibu kwenye majibu ya msingi, magari ya wagonjwa 195 yatanunuliwa katika mwaka huu wa fedha na yatapelekwa kwenye Halmashauri zote ikiwepo Halmashauri ya Babati Vijijini. Kwa hiyo, kituo hicho pia kitapata gari la wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Tabora Manispaa ina population kubwa ya watu zaidi ya 600,000; na pale Tabora Mjini kuna zahanati ambayo inazalisha watu 10 mpaka 20 kwa siku: Je, ni lini Serikali sasa itakuwa tayari ku-upgrade ile zahanati na kuwa kituo cha afya na kuiwekea wodi wa wazazi pamoja na theatre? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa
Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Munde, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafanya tathmini ya maeneo ambayo yana zahanati, lakini yana idadi kubwa ya wananchi na yana umbali mkubwa kutoka kituo cha afya au hospitali. Tutafanya tathmini kwenye zahanati hii aliyoisema ili tuone kama inakidhi vigezo iweze kupandishwa hadhi kuwa kituo cha afya.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Hospitali ya Mama na Mtoto, Chanika ina upungufu wa general wards za wanaume, wanawake na watoto ili kukifanya kituo cha afya kitoke kwenye hadhi ya kituo cha afya kuwa hospitali: Je, ni lini Serikali itajenga wodi hizi ili kuweza kuwasogezea huduma karibu wananchi wa Kata za Zingiziwa, Chanika, Mkuyuni, Kongola na Pugu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Jimbo la Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Mama na Mtoto ya Chanika ni hospitali ambayo inatoa huduma kwa akina mama lakini ina uhitaji wa wodi ya akina mama wajawazito na wodi ya watoto. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafanya tathmini na pia tunatafuta fedha kwa ajili kwenda kujenga wodi katika hospitali ile ya Chanika ili sasa iweze kuwa na miundombinu yote kwa ajili ya kulaza akina mama na mtoto. (Makofi)
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa hii nami niulize swali moja la nyongeza. Kwa kuwa sisi tuna vituo vya afya vya siku nyingi; Mkongo Gulioni, Mputa na Lusewa na havina vyumba vya upasuaji na wala Wodi ya Mama na Mtoto na vimechakaa sana: Je, Serikali inaweza kuwahakikishia wananchi wa Mkongo Gulioni, Mputa na Lusewa kama wapo katika list ya kukarabatiwa vituo vyao vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Natumbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatambua kwamba vituo hivi vya afya na vilivyo vingi nchini ni vya zamani ni vituo ambavyo vina upungufu wa miundombinu hususan majengo ya upasuaji na wodi. Ndiyo maana katika jibu la msingi nimesema, tunafanya tathmini kwenye vituo vya afya vyote ambavyo vina upungufu mkubwa wa miundombinu hasa majengo ya upasuaji na wodi ili baadaye tutafute fedha kwa ajili ya kuhakikisha majengo hayo yanajengwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge katika Jimbo la Namtumbo na vituo vya afya ambavyo amevitaja, tutavipa vipaumbele.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nataka kujua, ni lini Serikali italeta fedha katika Kituo cha Afya cha Kisaki ambacho kimejengwa kwa nguvu za wananchi na Kituo cha afya cha Mwaja ambacho kilipokea shilingi milioni 250 za mwanzo?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mussa Sima, Mbunge wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawapongeza sana wananchi katika hicho kituo hicho cha afya ambao wamechangia nguvu zao na wanasubiri kuungwa mkono na Serikali. Niwahakikishie Serikali inatambua sana nguvu za wananchi na tutatafuta fedha, ikipatikana twende tukaunge mkono nguvu za wananchi kuhakikisha vituo vya afya vinakamilika. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Hospitali ya Mji wa Tarime inakabiliwa na changamoto ya chumba cha kuhifadhi maiti kutokufanya kazi kwa takribani zaidi ya wiki tatu; na ukizingatia Hospitali ya Mji wa Tarime inahudumia zaidi ya Wilaya tatu, kwa maana hiyo, ina maana ina wagonjwa wengi, hivyo inakuwa na maiti nyingi ambazo zinahitajika kupelekwa Kituo cha Afya cha Sirari. Kwa sababu Halmashauri ya Mji wa Tarime haina fedha za kuweza kukarabati chumba kile cha kuhifadhi maiti, Serikali haiweze kuchukua jambo hili kwa udharura na kupeleka fedha ili kunusuru adha ambayo wanaipata Halmashauri ya Mji wa Tarime? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la jengo la kuhifadhia maiti kutofanya kazi katika Hospitali ya Mji wa Tarime, naomba nipokee taarifa hiyo na tutaifanyia kazi kwa haraka iwezekanavyo ili kuhakikisha wananchi wanaendelea kupata huduma hiyo muhimu katika hospitali hiyo.
MHE. ANNE K MALECELA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nikiri kwamba sijaridhika na majibu ya Serikali. Kwa kuwa anavyoongea Waziri ni kama kweli Kata ya Vunta kuna kituo cha afya, lakini Kata ya Vunta kuna jengo ambalo Serikali ililirithi kutoka maendeleo ya jamii mwaka 1962 miaka 60 iliyopita. Je, Serikali katika hali ya namna hiyo, naomba uniambie Mheshimiwa Waziri, tena kiukweli, mna mpango gani wa kujenga kile Kituo cha Afya cha Kata ya Vunta?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri Mkuu Ijumaa akimaliza kufunga Bunge hili mimi ninanyoosha, ninatangulia jimboni, wewe niambie unanifuata siku gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kwa namna ambavyo anapambana kuhakikisha wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wanapata maendeleo lakini pia huduma za afya. Nimhakikishie ni kwamba Serikali ilishafanya tathmini ya vituo vya afya vyote vyenye miundombinu pungufu ya kutoa huduma za afya. Tuna vituo vya afya ambavyo havina wodi na havina majengo ya upasuaji. Serikali tumeandaa database; na nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Kituo cha Afya cha Vunta ni miongoni mwa vituo ambavyo tayari vimeingizwa kwenye database na vitatengewa fedha mwaka wa fedha 2023/2024 na tutapanua majengo yale ikiwemo kujenga jengo la upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali hii sikivu ya Awamu ya Sita inafanya kazi hiyo na wananchi wa Same watapata huduma bora za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana la kufuatana na yeye, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge niko tayari kuongozana naye ili twende moja kwa moja Same tukapite Vunta na kuweka mpango kazi wa utekelezaji wa mpango huu.
MHE. FLATEI G. MASSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru Mheshimiwa Naibu Waziri alifika Mbulu Vijijini na Mheshimiwa Waziri kwenye Kata ya Maga. Je, ni lini watatuletea fedha kwa ajili ya kujenga kituo cha afya katika Kata ya Maga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tumefanya ziara zaidi ya mara katika Jimbo hili la Mbulu, lakini nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi nzuri anayoifanya, na Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kumalizia vituo vya afya ambavyo havijakamilika.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa vituo vya afya vipya tuangalie utaratibu baada ya kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya vya zamani lakini pia kupeleka vifaa tiba katika vituo hivyo.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nimeshawahi kuongea na Mheshimiwa Naibu Waziri mara kadhaa kuhusu kituo cha afya cha Une-Clinic Tabora, kwamba tunahitaji majengo ya upasuaji, theater na maabara ili kiweze kuwa kituo cha afya, kwa sasabu akina mama wajawazito wanazaa pale, kama akina mama 200 kwa mwezi.

Je, Serikali ni lini sasa itatuletea hizo fedha ili tuweze kukamilisha Kituo cha Afya cha Kaoni Clinic?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Munde, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mheshimiwa Munde amefuatlia suala Kituo cha Afya cha Town pale Tabora Manispaa; na alikuja pamoja na Mkurugenzi wa Manispaa, tulikubaliana wafanye tathmini ya ukubwa wa eneo lililopo ili tuweze ku-design michoro inayoweza kukaa pale ili tujenge jengo la ghorofa ili wananchi wa Tabora Manispaa wapate huduma.

Mhesimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kwamba zoezi hilo linaendelea litafanyiwa kazi na Serikali.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tabora Mjini lenye kata 29 ambalo ni kubwa sana kata nyingi za nje ambazo ni za vijijini zina upungufu mkubwa wa vituo vya afya, hasa katika Kata ya Uyui ambayo ina zahanati ambayo ingeweza Serikali ikaiboresha kuiweka kuwa kituo cha afya.

Je, Serikali inaahidi nini katika jambo hilo la kuzisaidia hizo kata za nje ya Mji wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli katika Manispaa ya Tabora kama ilivyo katika halmashauri zote kote nchini kuna upungufu wa vituo vya afya kwa baadhi ya kata. Dhamira ya Serikali ni kuhakikisha kwanza tunakamilisha ukamilishaji wa vituo vya afya vilivyoanza ujenzi na kupeleka vifaa vifaa tiba na watumishi ili vianze kutoa huduma za afya. Baada ya hapo tutafanya tathmini ya maeneo ambayo ni kimkakati kwa ajili ya kujenga vituo vya afya vingine ikiwemo katika eneo hili la Uyui.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nimekuwa nikiuliza swali hili mara kwa mara na nishukuru sana Serikali kwa sababu imetupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha upasuaji kwa ajili ya wanawake. Swali la kwanza; kwa kuwa Kituo hiki cha Afya cha Itaka kinatumika kama Kituo cha Afya cha Tarafa, kutokana na kwamba kata zote zinaunda Tarafa ya Itaka hazina vituo vya afya. Naomba kufahamu sasa ni lini Serikali itatupatia fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi za kawaida za watoto, wanaume pamoja na wanawake?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, mama yetu Mama Samia Suluhu Hassan alipokuja kwenye kampeni mwaka 2020 katika Kata ya Mlowo…

NAIBU SPIKA: Uliza swali Mheshimiwa Shonza.

MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, sawa. Naomba kufahamu sasa, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake aliyoahidi Mheshimiwa Rais wa Awamu ya kutujengea kituo cha afya katika Kata ya Mlowo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Shonza amekuwa akiulizia sana suala la Kituo cha Afya cha Itaka akishirikiana na Mheshimiwa Mbunge Mwenesongole, lakini nimhakikishie Serikali sikivu ya Awamu ya Sita, chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, imepeleka fedha hizo na kazi ya ujenzi wa jengo la upasuaji inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie kwamba Serikali inajenga vituo vya afya hivi kwa awamu, tumeanza majengo hayo ya awali, lakini fedha itatafutwa kwenda kujenga wodi ya wanawake, watoto na wanaume.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na ahadi ya Mheshimiwa Rais, kujenga Kituo cha Afya katika Kata ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja, nimhakikisie kwamba ahadi za viongozi wetu ni kipaumbele. Kwa hiyo, Serikali tayari imeshaanza kufanya michakato ya kuhakikisha kwamba tunapata fedha kwa ajili ya kujenga kituo hicho cha afya. Ahsante.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza, naishukuru Serikali kwa majibu mazuri, lakini ripoti ya CAG mwaka 2020/2021 imeonesha kwamba fedha hizi zimekuwa nyingi zikipotea kutokana na kutorejeshwa ipasavyo: Je, Serikali inatoa tamko gani kuhakikisha fedha hizi zinarejeshwa ili ziweze kuwanufaisha wanufaika wengine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika mwaka wa fedha 2020/2021 na miaka ya fedha ya nyuma ya mwaka wa fedha huo, kulikuwa na kasi ndogo ya urejeshaji wa fedha za mikopo ya asilimia 10, na Serikali ilitambua changamoto hiyo, tukachukua hatua; kwanza, kwa kuongeza usimamizi na uratibu wa mikopo pamoja na marejesho ya fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, nilijulishe Bunge lako Tukufu sasa kwamba mwenendo wa marejesho wa fedha hizi kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 umeongezeka kwa takribani asilimia 84 sasa ikilinganishwa na miaka nyuma ambayo ilikuwa chini ya asilimia 50. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, dhamira ya Serikali ni kuhakikisha tunaendelea kusimamia marejesho ya fedha hizi ili mfuko huu uendelee kuzunguka kunufaisha vikundi vingine.

Mheshimiwa Spika, nitoe tamko kwamba Wakurugenzi wa halmashauri zote kote nchini wahakikishe wanakopesha asilimia 10 kwa makundi yale kadri ya sheria, na wahakikishe wanarejesha fedha zile ili ziendelee kuwanufaisha wananchi wengine. Ahsante sana.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa kuna kundi kubwa la watu ambao sio vijana, wenye umri wa miaka ya 35 hadi 45, wanaachwa sana na ni changamoto kwenye ajira, na bado wapo kwenye kundi la kuajiriwa na Serikali kwa maana hawajafikia ukomo.

Je, ni lini Serikali sasa itarekebisha hiyo sera au itatoa tamko kwamba sasa nao wale watu wapewe mikopo kupitia hiyo asilimia kumi, au kuongeza asilimia 10 ili kupunguza hili wimbi la ukosefu wa ajira? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mikopo hii inatolewa kwa vijana ambao wana umri wa miaka 18 hadi 35 kwa mujibu wa definition ya vijana kwa utaratibu huu wa mikopo ya ten percent. Ni kweli kwamba kuna vijana ambao wana umri wa zaidi ya umri wa miaka 35 ambao pia wangeweza kunufaika na mikopo hii. Kwa hiyo, naomba niichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge tukaifanyie kazi na kuona uwezekano huo na pia kuona kama inaweza ikatekelezwa ama vinginevyo. Ahsante.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa Halmashauri za SMT ndiyo zinasimamia mikopo kwa ajili ya vijana, akina mama na walemavu; na kwa upande wa Zanzibar vilevile Halmashauri za SMZ zinasimamia hivyo hivyo: -

Je, Mheshimiwa Waziri kwa sababu halmashauri za bara tayari zinafanya kazi hiyo, lakini halmashauri ya Zanzibar kisheria zinatakiwa nazo zifanye kazi hiyo; utazisaidia vipi ili halmashauri zile ziweze kuwasaidia akina mama nao waweze kujikwamua katika maisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Fakharia Khamis, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, usimamizi wa mikopo ya asilimia 10 kwa maana ya Tanzania Bara, unasimamiwa na halmashauri; na kama ambavyo amesema Mheshimiwa Mbunge kwamba Zanzibar pia inatakiwa isimamiwe na halmashauri lakini kuna changamoto.

Mheshimiwa Spika, naomba kama Serikali tuchukue hoja hiyo ili tuweze kukaa pamoja tuone namna gani tunaweza tukaboresha kwa upande wa Zanzibar pia ili huduma hiyo iweze kuimarika. Ahsante sana.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na yote hayo utaona kwamba Hospitali ya Temeke sasa hivi ni hospitali ya Kimkoa. Kwa nini, sasa basi isiwe muhimu kituo hiki cha afya cha Malawi kipandishwe nakuwa Hospitali ya Temeke kwa sababu ile ya Temeke ni ya Kimkoa sasa hivi?

Swali la pili; Je, ni lini sasa Serikali itatutengea fedha ili tuweze kujenga mochwari katika kituo hiki cha Malawi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dorothy Kilave Mbunge wa Jimbo la Temeke kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Dorothy Kilave kwa namna ambavyo anawasemea kwa dhati kabisa wananchi wa Jimbo la Temeke, nimhakikishie kwamba katika utaratibu ambao Serikali inaendelea kuufanya kila Halmashauri lazima iwe na hospitali ya Halmashauri, ni kweli kwamba hospitali ya Temeke ni Hospitali ya Rufaa ya Mkoa kwa hiyo taratibu zitafanyika kufanya tathmini ya kituo cha afya cha Malawi kama eneo linatosheleza ili miuondombinu iongezwe ili baadaye iweze kupandishwa hadhi kuwa hospitali ya Halmashauri ya Temeke.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na jengo la mochwari tumeelekeza Halmashauri ya Manispaa ya Temeke ianze kutenga fedha kwenye mapato ya ndani, ili ijenge jengo la kuhifadhia maiti na huduma hiyo iweze kuwa bora kwa wananchi wa Temeke.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe ina tatizo kubwa sana la mashine ya X-Ray ni lini Serikali itapeleka mashine yakisasa ya X-Ray kwenye Hospitali ya Wilaya ya Ukerewe? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Mkundi Mbunge wa Jimbo la Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vifaa tiba zikiwemo X-Ray za kisasa ni moja ya vipaumbele ambavyo Serikali imeviweka na tunakwenda kwa awamu. Ninafahamu kwamba Hospitali ya Ukerewe ina X-Ray ya zamani ambayo imekuwa inaharabika mara kwa mara na Mheshimiwa Mbunge amekuwa mara kwa mara akikumbusha na kuomba Serikali iweze kupeleka X-Ray hiyo.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba tunaendelea kutafuta fedha na ni kipaumbele tukipata fedha tutahakikisha tunapeleka X-Ray katika kituo cha afya hicho.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, Serikali lini itakamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Ubungo iliyopo Kata ya Kimara ili iweze kupokea wagonjwa wa aina zote badala ya kupokea wagonjwa wa OPD ilivyo sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilipeleka fedha takribani shilingi bilioni moja na milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo na kazi ile inaendelea, nimefanya ziara pale zaidi ya mara tatu na huduma za awali zimeanza kutolewa.

Mheshimiwa Spika, hospitali ile itakamilishwa kwa fedha za awamu ya pili ambazo zitakwenda kukamilisha miundombinu ambayo imebaki.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera haina Mtaalam wa Mifupa na wagonjwa wanalazimika kupewa rufaa kwenda Bugando na hivyo kuwa na gharama kubwa.

Je, ni lini Serikali itapeleka Mtaalam huyo kuwasaidia wananchi?(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hospitali zetu zote za Rufaa za Mikoa zimewekea mpango mkakati kwanza kwa kuhakikisha Wataalamu na Madaktari Bingwa wa yale magonjwa ambayo ni kipaumbele sana ikiwemo matatizo ya mifupa wanakuwepo. Kwa hivyo, tunapokea hoja ya Mheshimiwa Mbunge ili tuifanyie kazi kama Serikali tupate Daktari kwa ajili ya Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Kagera.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, assante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wetu wa Tabora na hasa Tabora Manispaa, bado wagonjwa wengi wa rufaa wanakwenda Bugando kwa sababu ya kuwa na upungufu mkubwa wa Madaktari Bingwa katika hospitali yetu ya rufaa ya Kitete, sijui Serikali ina mpango gani wa kutuletea Madaktari Bingwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu swali la Mheshimiwa Rwamlaza, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha hospitali zetu za Rufaa za Mikoa zinakuwa na Madaktari Bingwa. Kwa hivyo, nimhakikishiwa Mheshimiwa Mbunge kwamba Hospitali ya Mkoa wa Tabora nayo ni kipaumbele na tutahakikisha tunapata wataalam hao kwa ajili ya huduma katika hospitali ile.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kituo cha afya cha Kata ya Malolo ni zaidi ya kilomita 150 mpaka hospitali ya Wilaya na kile kituo kimejengwa kwa nguvu ya wananchi na Waziri Mkuu amekichangia sana.

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba ili kituo hiki cha afya kianze kufanya kazi katika ubora wake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) : Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo Mbunge wa Jimbo la Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ninawapongeza wananchi wa Kata ya Malolo kwa kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao na Serikali imeendelea kuhamasisha wananchi kujenga vituo hivi kwa nguvu zao, Serikali ichangie nguvu za wananchi.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba katika mipango ya kuhakikisha vituo hivi vinapata vifaa tiba, tumeanza na Hospitali za Halmashauri lakini tutakwenda kwenye vituo vyetu vya afya ili vitoe huduma na kituo hicho pia kitapewa kipaumbele.
MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kituo cha afya cha Maskati Mkoani Morogoro kina Mhudumu mmoja wa afya. Je, ni lini Serikali itapeleka Wahudumu wa Afya katika kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwamba katika vituo vyetu vyote tunafahamu nchini kote kuna upungufu wa watumishi, ndiyo maana wiki iliyopita Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Utumishi, alitoa tangazo kwamba tutakwenda kuendelea kuajiri watumishi wa kada ambalimbali ikiwepo wa afya, nikuhakikishie kwamba tutatoa kipaumbele katika kituo cha afya ambacho kinahitaji mhudumu wa afya.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante Mheshimiwa Spika, wakati wa ziara ya Mheshimiwa Rais Mkoani Mara mwezi wa Pili mwaka huu, alielekeza kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda iweze kujengwa. Je, ni lini Serikali itajenga hospitali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kajege Mbunge wa Jimbo la Mwibara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni maelekezo ya kuyafanyia kazi mapema iwezekanavyo na tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeshaanza kuweka taratibu ili tuanze ujenzi wa hospitali katika Jimbo la Mwibara. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba suala hilo tayari linafanyiwa kazi.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Kwanza naishukuru Serikali kwa kuweza kutupatia fedha hiyo na ujenzi unaendelea. Ila sasa kwa kuwa fedha hii inakuja kwa mafungu ya shilingi milioni 500, na kwa kuwa fedha inayotakiwa kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Ngara ni shilingi bilioni tatu na zaidi.

Je, Serikali ipo tayari kuongeza muamala kutoka shilingi milioni 500, mpaka shilingi bilioni moja ili tuweze kujenga hospitali yetu kwa wakati na tuimalize? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kupeleka fedha kwenye Halmashauri hii ya Ngara kwa ajili ya ujenzi wa hospitali. Tayari wana bilioni moja; shilingi milioni 500 bado hawajaanza kuitumia. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba mara watakapotumia fedha hiyo kwa wamu ya pili, Mheshimiwa Rais na Serikali yetu itaendelea kupeleka fedha hiyo ili kuhakikisha Hospitali ya Halmashauri ya Ngara inakamilika.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi pia.

Mheshimiwa Spika, tatizo la Ngara ni sawa na tatizo lililoko Biharamulo maana tumeanza ujenzi wa hospitali ya Wilaya kwa muda mrefu sana, na kuna pesa milioni 204 ilirudishwa, nimeshaiongelea humu zaidi ya mara tano, lakini pia kuna pesa ya bajeti ya mwaka huu milioni 750. Sasa, kwa sababu hospitali hii tumeanza kuitumia tarehe 13 Januari, ila majengo mengine hayajamalizika.

Ni lini mtapeleka pesa hizi ili wananchi wa Biharamulo waweze kutumia Hospitali yao kwa uhuru ili wapate huduma wanayostahili kupata? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kupeleka fedha Biharamilo kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri kwa awamu, lakini nafahamu kuna fedha ambazo Mheshimiwa Chiwelesa amekuwa akifuatilia ili kuhakikisha kwamba fedha hizo zinatafutwa, zinapelekwa Biharamulo ili hospitali ile ikamilike ianze kutoa huduma kwa wananchi, ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Arusha ina Hospitali ya Wilaya ya Oltrument ambayo tangu Serikali ilipoanza kuboresha Hospitali za Wilaya Hospitali hii haijawahi kukumbukwa hata siku moja.

Je, ni lini Serikali itaona sasa umuhimu wa kuongeza majengo haya katika hospitali hiyo ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais tangu mwaka 2012? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Saputu Molllel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Arusha inanendelea na ujenzi na ina upungufu wa majengo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kujenga majengo hayo kwa awamu na Hospitali hii pia itapelekewa fedha ili iweze kukamilisha majengo yote muhimu. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; ni lini Serikali itatenga na kupeleka fedha kwa ajili ya kujenga majengo tisa muhimu ya kutolea huduma za afya katika Hospitali yetu ya Halmashauri ya Handeni Mjini, ili kuipa hadhi iwe sawa na Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Jimbo la Handeni Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali imeshapeleka shilingi milioni 900 katika Halmashauri ya Handeni Mjini, kwa ajili ya kuanza upanuzi wa Hospitali hiyo. Nimuhakikishie kwamba zoezi hilo ni endelevu ili tuhakikishe majengo yote tisa yanajengwa na huduma bora zinatolewa kwa wananchi wa Handeni Mjini.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; hospitali mpya ya Wilaya ya Kwimba iliyoko Icheja ina upungufu mkubwa wa miundombinu ambapo hakuna wodi za Watoto na akina mama na huduma mbalimbali hazipatikani, hivyo kupelekea usumbufu mkubwa kwa wagonjwa kuhitaji kupata huduma katika Hospitali mpya na huduma zingine katika kituo cha afya cha Ngudu, ambapo husababisha gharama kubwa sana za matibabu kwa wagonjwa.

Je, ni lini Serikali sasa itapeleka pesa za kutosha ili kukamilisha huduma za msingi zipatikane katika jengo moja kwenye hospitali mpya ya Icheja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyogeza la Mheshimiwa Kasalali Mageni, Mbunge wa Jimbo la Sumve kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa hospitali zetu za Halmashauri unakwenda kwa awamu, na kila baada ya awamu majengo kadhaa yanayokamilika yanaanza kutumika na majengo mengine yanapelekewa fedha kwa ajili ya ujenzi na kuanza kutumika. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Halmashauri hii ya Kwimba ni miongoni mwa Halmashauri ambazo zimewekwa kwenye bajeti, kuongezewa fedha ili miundombinu mingine ikamilike kwa ajili ya kutoa huduma, ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa hospitali yetu ya Wilaya ya Nyang’hwale inaendelea kukamilishwa na Mkurugenzi anatumia lile jengo la utawala.

Je, Serikali inatuambia nini kuhusu kumuhamisha Mkurugenzi huyo ili hospitali hiyo ianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli hospitali imekamilika, lakini kwa sababu ya ukosefu nwa jengo la utawala katika Halmashauri hiyo naomba nilichukue hili tutalifanyia kazi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuhakikishe Hospitali hii sasa inaanza kutoa huduma na isitumike kama jengo la utawala katika Halmashauri hiyo. Ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi ya swali la nyongeza.

Kwanza nishukuru Serikali ya Awamu ya Sita ya Rais Samia kwa kutupatia shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati wa majengo katika Hospitali yetu ya Wilaya pale Kinyonga, Kilwa Kivinje. Hata hivyo bado hali ya wodi zetu ni mbaya. Serikali ina mpango gani wa kuipatia fedha Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kwa ajili ya kujenga na kukarabati wodi pale Hospitali ya Wilaya Kivinje?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mmheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imekwishakupeleka shilingi milioni 900 ili kiufanya upanuzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa almaarufu Kinyonga; na zoezi hili linakwenda kwa awamu. Baada ya shilingi milioni 900 kutumika na kukamilisha majengo ya awamu ya kwanza Serikali itaendelea kupeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha majengo mengine. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Moshi ilipata shilingi milioni 500; mwaka wa fedha ulipita na mwaka huu wa fedha ilipata shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo mpaka sasa ujenzi huo haujaanza kutokana na kutokuwepo na mawasiliano mazuri kati ya TAMISEMI, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Wizara ya Fedha. Sasa ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwishatoa maelekezo kwamba fedha za miradi ya maendeleo zikiwemo za ujenzi wa hospitali zikishapelekwa katika Halmashauri ujenzi unatakiwa kuanza mara moja ili kupeleka huduma kwa wananchi. Naomba kutumia fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi kuhakikisha wanaanza ujenzi wa hospitali hiyo mapema iwezekanavyo ili dhamira ya Serikali ya kuwahudumia wananchi iweze kutimia, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; naomba kupata maelezo, Hospitali ya Wilaya ya Bunda tumepokea shilingi 3,650,000,000 na haina dalili za kumalizika, na Mheshimiwa Naibu Waziri ulikuja juzi ukaiona. Ni lini itamalizika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imepeleka zaidi ya shilingi 3,200,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda; na wiki mbili zilizopita nilifanya ziara katika Halmashauri hiyo pamoja na Mbunge. Tulikubaliana, kwanza tunachukua hatua za kinidhamu kwa wataalam wote waliosimamia hospitali ile na kupelekea kutokukamilika kwa majengo ilhali fedha zilishapelekwa.

Pili, tumekubaliana kwamba fedha itapelekwa ili ikamilishe majengo yale mapema iwezekanavyo na huduma za afya zianze kutolewa, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti nashukuru, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini mazingira pale kwenye lile soko na fedha zinazobadilishwa wakati wa biashara pale ambazo ni nyingi sana zinahitaji kuweka miundombinu ikae vizuri kidogo.

Je, Serikali iko tayari kwenda kujenga shade kama machinga complex ya Dodoma pale kwa ajili ya kunusuru akina mama ambao wanachomwa na jua wakati wa jua kali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Halmashauri ilitumia takribani Milioni 11 kwa ajili ya kuweka stendi ndogo pale ambayo inaweza ikaingiza mabasi 12. Je, Serikali haioni kwamba ni muhimu sasa kuingilia kati na kujenga ile barabara ya kutokea kwa sababu kibali cha kutumia ile stendi bado hakijatoka kutokana na barabra kutokukidhi viwango. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufatilia suala la soko lile la Tengeru, lakini utaratibu wa Serikkali ni kwamba tumetafuta eneo jingine kubwa zaidi haina maana kwamba tunaliacha kabisa lile eneo ambalo tayari kwa sasa linatumika kama gulio. Kwa hiyo, ninatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri hii ili watenge fedha kwenye mapato ya ndani kuboresha soko hilo, kwa maana kuweka miundombinu rafiki kwa wafanyabiashara, pia kupitia TARURA Halmashauri hii watenge fedha kwa ajili ya kuboresha barabara hiyo ambayo itawezesha kujenga uwezo wa wananchi kufanya biashara kwa ufanisi mkubwa zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa baadhi ya watu wenye ulemavu wanapata changamoto ya kufanya biashara wakiwa peke yao pengine kutokana na nature na ile hali ya ulemavu wao na kwa kuwa imejidhihirisha kwamba Halmashauri nyingi zinakosa wakopaji wa kutosha katika kundi hili la walemavu na hivyo kupelekea zile fedha kukopeshwa kwenye makundi mengine au hata kurudishwa. (Makofi)

Je, Serikali ina mpango gani basi wa kuwarahisishia zaidi hawa watu wenye ulemavu ili waweze kutumia ile asilimia mbili yao ambayo wamewekewa kwa mujibu wa sheria? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Anania Tadayo, Mbunge wa Jimbo la Mwanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kasi ya ukopaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa kundi la watu wenye ulemavu bado hairidhishi na Serikali tumeona hilo na moja ya sababu ni kwamba walio wengi hawana ile confidence ya kukopa wakiamini kwamba hawawezi kurejesha. Lakini ni hatua ambazo Serikali imechukua kwanza ni kuendelea kutoa elimu na hamasa kwa watu wenye ulemavu; lakini pili kuwarahisishia kwamba hata mtu mmoja mwenye ulemavu anaweza akapata mkopo wa asilimia 10 akafanya biashara yake baada ya Kamati ya Mikopo kujiridhisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nitumie fursa hii kuhamasisha wananchi, lakini kuwaelekeza watendaji kuendelea kuhamasisha na kutoa elimu kwa makundi ya watu wenye ulemavu ili wapate mikopo ya asilimia 10, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa shida kubwa sana inayopata watu wenye ulemavu hasa wenye uoni hafifu, Serikali haioni umuhimu sasa wa kutengeneza document zenye nukta nundu ili hawa watu wanaopata shida ya kusoma waweze kujua taarifa za mikopo katika Halmashauri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja hii ni muhimu na sisi tunaichukua kwa ajili ya kuifanyia kazi ili kukwawezesha watu wenye ulemavu au uoni hafifu waweze kupata uwezo wa ku-access taarifa hizo kupitia taarifa za nukta nundu, ahsante sana.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali kwa sababu imekuwa ni kilio cha muda mrefu kupata stendi ya kisasa katika Mji wetu Ikungi. Sasa. ili kujiridhisha, ni hatua gani sasa zimeanza kuchukuliwa katika kuanza ujenzi huu mapema?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa fedha zilizotengwa, kwa maana milioni 110, ni fedha kidogo. Nini mkakati wa kuongeza fedha za kujenga stendi yenye hadhi ili tuweze kuwa na stendi kubwa kwa sababu ni main road na inapokea magari mengi yanayoelekea Dar es Salaam na Mwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna uhitaji wa stendi katika eneo hilo la Ikungi, na tayari shughuli za awali za ujenzi ikiwemo kusafisha eneo lakini pia kufanya upembuzi imeshaanza kwa ajili ya kuanza ujenzi huo; na tunaamini shilingi milioni 110 itaanza kazi katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, lakini tathmini iliyofanyika inahitaji shilingi milioni 700 ili kukamilisha stendi hii ya Ikungi. Tumeshakubaliana kama Serikali kupitia mapato ya ndani ya halmashauri kila mwaka watatenga shilingi milioni 150 na katika mwaka ujao wa fedha 2023/2024 halmashauri imakwishatenga fedha hiyo kwa ajili ya kuendelea na ujenzi ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais mwaka jana alipotembelea Mji wa Lamadi aliahidi ujenzi wa stendi. Je, ni lini ujenzi huu sasa utaanza ili kuokoa maisha ya watu kwa sababu ya msongamano mkubwa ulioko pale?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe Lusongekile, Mbunge wa Jimbo la Busega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Rais Daktari Samia Suluhu Hassan alielekeza mamlaka za Halmashauri ya Busega kuanza mpango wa kujenga stendi katika eneo la Lamadi. Ofisi ya Rais TAMISEMI tumekwishamwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Busega kufanya tathmini na kuandaa makadirio ya gharama kwa ajili ya kuanza ujenzi huo. Kazi hiyo inaendelea watawasilisha Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya hatua zaidi, ahsante.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongea.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu Mkoa wa Songwe ni Mkoa Mchanga na una uhitaji wa stendi kuu ya mkoa. Serikali imefikia hatua gani katika kuhakikisha ujenzi wa stendi hii unakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwishatoa maelekezo na utaratibu wa mikoa yote na halmashauri zote ambazo zina uhitaji wa miundombinu ya stendi kuandaa maandiko pamoja na kufanya tathmini ili kuziwasilisha Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya kuwasilisha Wizara ya Fedha na Mipango ili kuona kama inakidhi vigezo vya kuwa miradi ya kimkakati yatafutiwe fedha lakini kama hayakidhi basi kupitia vyanzo vingine vituo hivyo viweze kujengwa. Kwa hiyo naomba nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalifanyia kazi suala la stendi ya Mkoa wa Songwe na utekelezaji utafanyika, ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ile stendi ya Musoma Mjini Manispaa kipindi kama hiki cha mvua huwa inabadilika badala kuwa stendi inakuwa sawasawa na zizi, kwa maana tope zinajaa. Kwa kuwa Serikali ilishaahidi kuijenga tangu mwaka 2020 ni lini hiyo stendi itajengwa ili na sisi watu wa Musoma tuweze kuwa na stendi nzuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Jimbo la Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba stendi ya Manispaa ya Musoma ni mbovu na Serikali imeshachukua hatua kwanza kwa kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Musoma kuandaa tathmini ya mahitaji ya gharama za ujenzi, lakini pia kuanza kutenga fdha kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kote nchini kwamba kunapohitajika miundombinu muhimu kama hii lazima wafanye tathmini, waanze kutenga fedha za mapato ya ndani asilimia 40 au 60 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa miradi kama hii ili kuondoa changamoto kwa wananchi, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Mradi wa Miji 45 utakaoboresha miji 45 maarufu kwa jina la TACTIC, sehemu mojawapo ni pamoja na ujenzi wa barabara, lakini pia pamoja na ujenzi wa stendi ambazo zitakuwa chanzo cha mapato cha Halmashauri zetu likiwemo pia Jiji la Mbeya. Je, ni lini mradi huo utaanza ili kuwezesha Halmashauri na Miji hiyo kuwa na stendi za uhakika ambazo zitakuwa pia chanzo cha mapato?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Miradi ya TACTIC imegawanywa katika phases tatu. Tier one, two and three, lakini tier one hatua zinaendelea, tier two na three pia hatua zinaendelea ili kuhakikisha katika kipindi hicho miradi yote hii inatekelezwa kwa kuboresha barabara, masoko lakini pia na stendi katika miji hiyo 45. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mafinga pia itatekelezewa mradi huo kama ilivyopangwa kwenye mpango wa TACTIC, ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Stendi iliyopo katika Wilaya ya Karatu haikidhi vigezo na hasa wakati wa masika inakuwa na changamoto kubwa. Je ni lini Serikali itajenga stendi ya kisasa tukizingatia karatu ni mji mdogo wa kitalii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, uhitaji wa stendi katika Halmashauri ya Karatu ni muhimu na ni kweli kwamba kuna uhitaji huo, lakini tumekwishamwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Karatu kufanya tathmini ya gharama, lakini kama gharama ni kubwa juu ya uwezo wa halmashauri, walete kama mradi wa kimkakati, lakini tunasisitiza halamashauri kutenga fedha za mapato ya ndani kuanza kukarabati stendi hii ya karatu, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kujibu maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya Halmashauri zimekuwa kubwa mno na nyingine zimekuwa zina maeneo makubwa sana kijiografia, lakini nyingine zina Majimbo matatu, nyingine zina Majimbo mawili na kupata huduma wanapata katikati ambako ni Mjini.

(i) Je, serikali sasa haioni haja ya kufuata uhalisia na urahisi wa kupata huduma katika ugawaji wa Halmashauri hizo?

(ii) Je, ni nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba katika utengaji wa fedha za maendeleo jiografia za Halmashauri zetu iwe ni mojawapo ya kigezo cha kuzingatiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali wawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tuna Halmashauri ambazo zina maeneo makubwa kijiografia, lakini kuna Halmashauri ambazo zina Majimbo zaidi ya moja na ni kweli kuna changamoto ya umbali kutoka baadhi ya maeneo ya Halmashauri kufika kwenye Makao Makuu ya Halmashauri hizo. Serikali kwa sasa sote ni mashahidi kwamba mamlaka nyingi zimeanzishwa hazina majengo muhimu ya utawala, hazina miundombinu muhimu ya huduma za jamii. Kwa hiyo, kipaumbele cha Serikali kwa sasa ni kukamilisha kweye mamlaka zilizopo na baada ya hapo taratibu zitafuatwa ili kupata mamlaka nyingine na kusogeza huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili; Serikali imekuwa ikipeleka fedha kwa kuzingatia jiografia kwa maana ukubwa wa maeneo, ndiyo maana hata kwenye Mfuko wa Jimbo, kigezo mojawapo ni ukubwa wa eneo la Halmashauri husika lakini hata kwenye fedha za barabra kwa maana ya TARURA kigezo mojawapo ni hicho. Kwa hiyo, Serikali inazingatia pia ukubwa wa kijiografia wa maeneo husika. Ahsante. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Maeneo yote hayo mawili ya Sirari na Nyamongo ni ahadi za Viongozi Wakuu wa Serikali, sasa nimuombe Mheshimiwa Waziri kama yupo tayari majibu haya haya tuyapeleke pale Sirari na Nyamongo akayaseme mwenyewe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, nipo tayari tuongozane na Mheshimiwa Mbunge na bahati nzuri wiki mbili zilizopita tulikuwa Tarime Vijijini tumefanya ziara pamoja na niko tayari turejee tena Tarime kwenda Sirari na Nyamongo.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Katika Miji Midogo iliyoko nchini sasa hivi kumekuwa kuna sintofahamu kati ya Mamlaka ya Miji Midogo na Halmashauri kuhusu nani hasa akusanye mapato yapi? Je, Serikali sasa iko tayari kutoa mwongozo unaoeleweka ili mamlaka zote mbili zijue mipaka yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimejibu kwenye swali la msingi tuna mamlaka za Miji Midogo 71 kote nchini inawajibika katika Halmashauri Mama na inatekeleza majukumu yake chini ya usimamizi wa Halmashauri Mama. Kwa hiyo, haina mamlaka ya moja kwa moja mpaka pale itakapopata sifa ya kuwa Halmashauri ya Mji. Kwa hiyo, ikiwa Mamlaka ya Mji mdogo bado haina mamlaka ya moja kwa moja na wao siyo Accounting Officers, kwa hiyo tutaendelea kuhakikisha kwamba kwanza tunawawezesha kwa kuwajengea uwezo lakini ku-harmonize mahusiano kati ya Halmashauri Mama lakini na Mamlaka za Mji Mdogo. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niishukuru Serikali, kwa kuamua kwamba itatenga shilingi Milioni 400 katika mwaka huu wa fedha 2023/2024 ili kukimalizia kituo cha afya cha Mchomoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa, sisi pia tuna vituo vitatu, Kituo cha Mkongo, kituo cha Rusewa na kituo cha Mputa vya afya, ambavyo ni vya siku nyingi sana. Tuliahidiwa katika Bunge lako tukufu hapa kwamba vitafanyiwa ukarabati.

Je, Serikali ni lini itafanyia ukarabati vituo vya afya vya Mkongo, Rusewa na Mputa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa Mbunge wa Jimbo la Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Namtumbo ina vituo hivi vitatu vya afya, amabvyo ni vya siku nyingi vimekuwa chakavu, Serikali imeweka mpango wa kuainisha vituo vyote chakavu lakini kutenga fedha kwa awamu, kwa ajili ya kuvikarabati. Kwa hiyo, ninakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge wakati tunatekeleza utaratibu huo, vituo hivi vya afya pia vitaingia kwenye mpango na kukarabatiwa kwa awamu. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, changamoto ya ufinyu wa maeneo ya kutolea huduma ya afya ya mama na mtoto hasa eneo la kujifungulia ipo maeneo mengi ndani ya Wilaya yangu ya Hanang.

Je, sasa Serikali haioni ni wakati muafaka kufanya tathmini ya jumla wakati tukiendelea kupanga mpango wa kujenga kituo cha afya kila Kata ili kufanya maboresho katika maeneo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili fedha zilizotengwa kwa zahanati ya Laghanga, milioni 10. Je, Serikali haioni kwamba hizo fedha ni kidogo haiwezi kutosheleza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba zahanati zile ambazo zilijengwa miaka ya nyuma zilikuwa ndogo na vile vyumba vya kujifungulia vilikuwa finyu lakini kwa sasa Serikali imeboresha sana ramani zetu, ramani zetu ni kubwa zina vyumba vya kutosha vya kujifungua, lakini pia vya kupumzika wakina mama baada ya kujifungua. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba kwa ramani za sasa tutajenga zahanati zenye nafasi za kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kujenga vituo vya afya kila Kata utaratibu wa Serikali tutajenga vituo vya afya vya kimkakati katika maeneo ya kimkakati ambayo yana idadi kubwa ya watu lakini umbali mkubwa kutoka kituo cha huduma cha Jirani zaidi. Lakini hii shilingi milioni 10 imetengwa kutoka mapato ya ndani na chumba kinakwenda kuongezwa katika jengo lile ambalo linatumika kwa sasa, kwa hiyo tunaamini itatosha na kama haitatosha basi Serikali itaongezea kuhakikisha kwamba chumba hicho kinakamilika. Ahsante. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha afya cha Nguvukazi - Chanika kinahudumia mama na mtoto na Serikali, ni lini sasa itaona umuhimu wa kujenga majengo wezeshi kama wodi za wanawake, wanaume na chumba cha kuhifadhia maiti ili kituo cha afya hiki kipate hadhi ya kuwa Hospitali na kuwahudumia wananchi wa Kata za Chanika, Buyuni, Zingiziwa na Msongola?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa JImbo la Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Kituo cha Afya hiki cha Chanika kinahudumia wananchi wengi na tulishatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Jiji la Dar es Salaam kwa maana ya Manispaa ya Ilala, kutenga fedha kati ya asilimia 60 kwa ajili ya kufanya upanuzi na ujenzi wa wodi katika kituo hiki. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi kwamba hiki ni kipaumbele cha wananchi ahakikishe anatenga fedha kwenye mapato ya ndani ili tuweze kujenga wodi hizo. Ahsante. (Makofi)
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu ya Serikali.

Kwa kuwa mchakato wa bima ya afya kwa wote umo mbioni kukamilishwa, na kwa kuwa miaka ya nyuma kulikuwa na utaratibu mzuri wa kwenda kuchunguza afya za watoto mashuleni kwa vipindi kadhaa kwa mwaka. Je, Serikali haioni umuhimu wa kurudisha mpango huu wa kuchunguza afya za vijana wetu shuleni walau mara mbili kwa mwaka, katika jitihada za kupunguza gharama kwa kugundua maradhi mapema ili kukinga na kuwapunguzia wanafunzi hawa shida au wazazi wao kupeleka hospitali wanapokutwa maradhi yameshawatokea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli ni muhimu sana kuwa na utaratibu wa ku-check afya za wanafunzi shuleni angalau mara mbili kwa mwaka, utaratibu huo uko kwenye miongozo yetu, ni kweli kwamba hapa katikati ufanisi wake umepungua kidogo. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwanza tumepokea ushauri wake tutakwenda kutekeleza, pia nitoe maelekezo kwa Wakuu wa Shule na Halmshauri zetu kuhakikisha wanaweka utaratibu kwa kutumia Waratibu wa Elimu, pia na Waratibu wa Huduma za Afya katika shule ili watoto wetu wachekiwe mara kwa mara afya zao na kupewa matibabu mapema. Ahsante. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kwanza niipongeze Serikali kwa kujenga vituo vya afya na hospitali ya Wilaya. Kwa bahati mbaya sana idadi ya watumishi ambao ndio wanaokuja kufanya kazi kwenye maeneo husika kwenye vituo vya afya na hospitali ya wilaya bado ni wachache, Halmashauri yangu ya Wilaya kwenye hospitali ya wilaya mahitaji ya watumishi ni 608 waliopo ni 40 tu, kitu ambacho wanashindwa kufanya kazi na wanashindwa kutoa huduma ile iliyokusudiwa.

Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itapeleka wahudumu hasa kada ya wauguzi ili waweze kufanya kazi na hospitali ya wilaya ianze kufanya kazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Serikali imeleta X- ray kwenye eneo la Wilaya ya Tanganyika, kinachokwamisha sasa hivi ni Bodi ile ya Mionzi kutokwenda kuthibitisha. Je, ni lini watawapeleka wataalam hao na hiyo X-ray ilishafungwa kama miezi minne iliyopita? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imejenga Hospitali ya Halmashauri ya Tanganyika na hospitali ile imeanza kutoa huduma za afya kwa awamu ya kwanza na watumishi waliopo 40 kwa sasa ni wale ambao wanatoa huduma za awali. Serikali imeweka utaratibu mzuri kuhakikisha kwamba majengo mengine yanapoanza kutoa huduma, watumishi pia wanapelekwa, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hawa watumishi 608 wanahitajika pale hospitali itakapoanza kutoa huduma katika majengo yote, lakini kwa sasa watumishi 40 wanatoa huduma zile za awali na Serikali itaendelea kupeleka watumishi ili waweze kutoa huduma zote katika wodi ambazo zinaendelea na ukamilishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na suala la x-ray ni kweli Serikali imepeleka digital x-ray katika Halmashauri ya Tanganyika kama ambavyo imepeleka katika Hospitali za Halmashauri nyingi kote nchini na wataalam wa mionzi kutoka Arusha tutawasiliana nao wafike Tanganyika ili waweze kufanya ukaguzi na kutupa kibali cha kuendelea na huduma za x-ray, ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa Serikali imejenga vituo vingi ikiwepo katika Jimbo la Makambako, Kituo cha Ikelu, Kitangililo na Lyamkena.

Je, ni lini sasa Serikali itatupelekea waganga ili kusudi wananchi waendelee kupata matibabu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Deo Kasinyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imejenga Vituo vya Afya vya Ikelu, Kitandililo na Lyamkena na nimpongeze sana Mheshimimiwa Deo Sanga, kwa namna ambavyo anawapigania wananchi wa Jimbo la Makambako na huduma za afya zimeendelea kuboreshwa. Nimhakikishie kwamba Waganga watapelekwa katika vituo hivi ili waanze kutoa huduma za awali za msingi wakati Serikali inaendelea kuajiri watumishi wengine kwa ajili ya kuwapeleka katika vituo hivi, ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kata ya Sunya katika Kituo cha Afya tulipata ajali mbaya sana mwezi Novemba na tulipoteza watumishi karibu sita, sasa kituo kinataka kufungwa. Je, ni nini commitment ya Serikali kuweza kutuletea watumishi hao kwa haraka sana ili kituo kisifungwe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Olelekaita, Mbunge wa Jimbo la Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ilitokea ajali na kupoteza watumishi wetu takribani sita katika Kituo cha Afya hiki cha Sunya. Mwenyezi Mungu azilaze roho za marehemu mahali pema peponi, lakini shughuli za Serikali lazima ziendelee katika kituo kile cha afya na tulikubaliana na Katibu Tawala wa Mkoa wa Manyara, kuhakikisha anafanya mgawanyo wa ndani wa watumishi waende kwenye kile kituo cha afya waanze kutoa huduma. Kwa hiyo, naomba nitumie fursa hii kumkumbusha Katibu Tawala wa Mkoa haraka iwezekanavyo apeleke watumishi kwenye kituo hiki cha afya ili wananchi waendelee kupata huduma za afya, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninalo swali la nyongeza.

Kwa kuwa mgonjwa anapofika hospitalini hawezi kupata matibabu sahihi bila kupata vipimo; je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha zahanati zote nchini zinapata maabara ili kutoa huduma sahihi kwa wagonjwa wetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ili upate huduma bora za afya lazima vipimo vya maabara vifanyike na Serikali kwanza imechukua hatua ya kuboresha ramani za majengo ya zahanati kwa kuongeza vyumba kutoka sita hadi vyumba 15, ambavyo vitawezesha kuwa na jengo zuri ambalo linakidhi huduma za maabara katika zahanati zetu.

Mheshimiwa Naibu Sspika, pili, zahanati zetu ambazo zilijengwa miaka ya nyuma ambazo hazikuwa na nafasi nzuri kwa ajili ya huduma za maabara, tumetenga maeneo ambayo huduma za maabara za msingi, kwa mfano vipimo vya malaria, vipimo vya wingi wa damu vinafanyika katika vyumba ambavyo vimekuwa improvised na huduma hizi zinaendelea kutolewa katika maeneo haya. Ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nakushukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunijibu swali langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ningependa kumuuliza Mheshimiwa Waziri; kwamba kutokanana changamoto kuwa kubwa ya migogoro ya wakulima na wafugaji kila kukicha ambayo imesababisha watu mbalimbali kupambana na kufa wengine, wengine wamepata ulemavu.

Je, haioni kwamba kuna uhitaji sasa wa kuharakisha huu mpango wa matumizi bora ya ardhi, ili vijiji bora 34 vilivyobaki viweze kumalizwa kupangwa katika huu mpango wa matumizi bora ya ardhi mwaka 2023/2024?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swalli la pili. Katika kipindi cha miaka 10 Takwimu za Sensa zimeonesha katika Wilaya ya Kilwa kumekuwa na ongezeko kubwa la wananchi. Mwaka 2012 tulikuwa na wananchi 190,744, mwaka 2022 takwimu za sensa zinaonesha kwamba wananchi wa Wilaya ya Kilwa wameongezeka hadi kufikia 297,676 sawa na ongeezeko la watu 106,932 sawa na asilimia 52 ya ongezeko. Kutokana na ongezeko hili ni wazi kwamba sehemu kubwa ya watu walioongezeka ni jamii ya wafugaji...

MWENYEKITI: Uliza swali.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Je, Serikali haioni sasa wakati umefika wa kuweza kuwahamisha baadhi ya wafugaji kutoka Wilayani Kilwa kwenda maeneo mengine ya nchi kama ilivyofanya katika Bonde la Ihefu na katika Hifadhi ya Taifa ya Ngorongoro?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna changamoto ya mogogoro kati ya wafugaji na wakulima katika Halmashauri ya Kilwa, lakini pia katika baadhi ya halmashauri hapa nchini. Serikali imeendelea kuchukua hatua, na hatua moja muhimu ni kupanga matumizi bora ya ardhi katika vijiji ili kuwa na maeneo mahsusi kwa ajili ya kilimo, pamoja nakuwa na maeneo mahsusi kwa ajili ya ufugaji lakini pia kutunza vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na katika Halmashauri ya Kilwa kama nilivyotangulia kusema tayari bajeti imeandaliwa ya milioni 60 kwa ajili ya kupitia mipango bora ya ardhi. Zoezi hili ni endelevu mpaka tutakapokamilisha vijiji vingine vilivyobaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili kuhusiana na ongezeko la wananchi ni kweli wafugaji wengi wamehamia Kilwa na Mkoa wa Lindi kwa ujumla na baadhi ya mikoa mingine. Serikali inaendelea kufanya tathmini na kuona maeneo yale ambayo yana wafugaji wengi basi tuweze kuweka mgawanyo sahihi ili kulinda mazingira lakini kuepusha migogoro, ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na napongeza sana Serikali ya Awamu ya Sita kwa maboresho makubwa, hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, moja; ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha hasa madaktari na wauguzi?

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; ni lini Serikali itapeleka vifaa vya kutosha katika Kituo cha Afya Chimara lakini pia Kituo cha Afya Igurusi ili waweze kutoa huduma za upasuaji? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshapeleka vifaa tiba vya shilingi milioni 418 katika Halmshauri ya Mbarali, lakini katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 69.65 kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba kwenye vituo vya afya na hospitali za halmashauri pamoja na zahanati zilizokamilika. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la kupeleka vifaa tiba kwenye vituo vyetu ni endelevu, lakini pia vituo hivi vya Mbarali vitapata vifaa tiba hivyo.

Mheshimiwa spika, lakini pili katika mwaka wa fedha uliopita Serikali iliajiri watumishi 10,462 na Halmashauri ya Mbarali ilipata watumishi 51 wakiwemo madaktari na wauguzi na Seriakli itaendelea kupeleka watumishi hao katika halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mbarali, ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Mapera kilichopo Mbinga Vijijini hakina vifaa tiba vya msingi ikiwemo ultrasound, x-ray na hamna generator hali inayozorotesha upasuaji hasa nyakati za usiku. Fedha ambazo Serikali imetenga, je, na Kituo cha Afya cha Mapera kimetengewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Judith Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kituo hiki cha afya cha Mapera kilichopo katika Halmashauri ya Mbinga ni moja ya vituo ambavyo vimeingia kwenye orodha ya kupelekewa vifaa tiba katika bajeti ya mwaka wa fedha huu 2022/2023, lakini pia tutaendelea kutenga katika bajeti ijayo ya 2023/2024, ahsante.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi.

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba mfano x-ray machine na ultrasound kwenye Vituo vya Afya vya Kamsamba, Mkulwe, Msangano, Ndalambo pamoja na Kapere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, Mbunge wa Jimbo la Momba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa taratibu na sera za afya, vituo vya afya vinapelekewa mashine za ultrasound lakini vituo vya afya ambavyo vinapata mashine za x-ray ni baada ya tathmini ya kuona idadi ya wananchi wanaotibiwa katika maeneo hyo.

Kwa hiyo, naomba nichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge, tufanye tathmni ya kuona idadi ya wananchi wanaotibiwa kaita Kituo cha Kamsamba na vingine ambavyo amevitaja kama vinakidhi sifa za kuwa na mashine za x-ray, lakini nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Momba kwamba mashine za ultrasound ziko ndani ya uwezo wa halmashauri kununua wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kuongeza nguvu katika maeneo hayo, ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kumekuwa na mkanganyiko kwa hizo pesa zilizopelekwa katika halmashauri kwa sababu wengine hawajui kama ziende kwenye vituo vya afya au kwenye zahanati.

Sasa Serikali haioni sababu ya kuweka maelekezo maalum kabisa kwamba hizi pesa either ziende kwenye kituo cha afya na hizi ziende kwenye zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela, Mbunge wa Jimbo la Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa zahanati au vituo vya afya au hospitali za halmashauri inapeleka na barua ya maelekezo kwa Mkurugenzi kwamba fedha zilizoletwa ni kwa ajili ya kujenga kituo cha afya eneo gani au zahanati eneo gani au hospitali ya halmashauri eneo gani?

Kwa hiyo, naomba nirudie kusisitiza kwa Wakurugenzi wa Halmashauri kwamba wazingatie maelekezo yanayotolea na Ofisi ya Rais, TAMISEMI mara fedha zinapopelekwa katika ujenzi wa vituo hivi, ili kuepuka mkanganyiko ambao Mhehimiwa Mbunge ameusema, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika,
ahsante sana kwa kunipa fursa.

Kituo cha afya cha Umbwe ambacho ni ndio kituo pekee cha afya katika Tarafa ya Kibosho hakina gari la kubeba wagonjwa; je, Serikali ina mpango gani wa kutupatia gari la kubeba wagonjwa katika kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Profesa Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimia Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Umbwe ni kituo pekee katika tarafa hiyo na kinahudumia wananchi wengi na hakina gari la wagonjwa. Mheshimiwa Ndakidemi amekuwa akifuatilia mara kwa mara, lakini naomba nikujulishe Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika mwaka huu wa fedha tutapeleka magari ya wagonjwa katika halmashauri zote 184, lakini pia tutapeleka magari ya huduma za afya kwa maana usimamizi katika halmashauri zote 184, ikiwemo Halmashauri hii ya Moshi Vijijini, na hivyo ni maamuzi ya halmashauri kuona inakipa kipaumbele kituo hiki cha afya cha Umbwe ili kiweze kupata gari hilo, ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante; je, ni lini Serikali hii itapeleka vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Bashnet na Madunga katika Jimbo la Babati Vijijini ambavyo viko tayari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, pamoja na Kituo hiki cha Afya cha Bashnet, lakini na vituo vingine vya afya ambavyo vimekamilika katika Jimbo la Babati Vijijini Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 69.95 katika mwaka huu wa fedha na tayari vifaa tiba vimeanza kupelekwa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatoa kipaumbele pia katika kituo hiki cha afya ili kiweze kupata vifaa tiba hivyo, ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na naishukuru Serikali kwa kutujengea vituo vya afya ndani ya Jimbo la Hai.

Swali langu, ni lini sasa Serikali itatuletea vifaa tiba kwenye Vituo vya Afya vya Kwansira, Chemka na pale Kisiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nafahamu kwamba Kituo cha Afya cha Kwansira ambako mimi na yeye tulifanya ziara na kazi ya ujenzi iko hatua za mwisho, ni sehemu ya vituo ambavyo vinahitaji vifaa tiba mara baada ya kukamilika, lakini pamoja na hivi vituo vya afya vingine ambavyo amevitaja. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kutenga fedha na kupeleka vifaa tiba kwenye vituo hivyo alivyovitaja ili kuendelea kutoa huduma bora kwa wananchi wa Hai, ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante, Kituo cha Afya cha Igalula katika bajeti tulikitengea milioni 450 na tumekwisha pokea milioni 450 lakini cha ajabu TAMISEMI mmeleta barua ya kugawa zile fedha kwenye vituo vitatu.

Je, kwa nini Serikali isione haja ya kukimaliza kabisa Kituo cha Afya cha Igalula katika vifaa tiba na kiendelee kutoa huduma stahiki? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant David Protas, Mbunge wa Jimbo la Igalula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwanza dhamira ya kwanza ni kuhakikisha kwamba vituo vile vinakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi mara moja.

Naomba sasa niichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imepeleka shilingi milioni 450 lakini kuna maelekezo ya kuzigawa fedha hizo katika vituo vitatu, nikitoka hapa nikaa na Mheshimiwa Mbunge lakini nifuatilie kuona sababu za msingi za kufanya hivyo na kama hakuna sababu tutakubaliana tukamilishe Kituo cha Afya cha Igalula na hatimaye tuendelee na vituo vingine kwa mujibu wa utaratibu, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. THEA M. NTARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwanza, nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista kwa kazi nzuri anayoifanya katika kile kijiji kwenye zahanati.

Je, ni lini sasa Serikali mtapeleka vifaa tiba kwenye Zahanati ya Mdunduwaro ili ianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika,
ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Ntara lakini nimpongeze sana Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa namna ambavyo wameendelea kusimamia ujenzi wa Zahanati ya Mdunduwaro na ni kweli kwamba Mheshimiwa Jenista Mhagama amekuwa akilifuatilia na Mheshimiwa Dkt. Thea Ntara amekuwa akilifuatilia.

Nimhakikishie kwamba tulishakubaliana kwamba kwanza Zahanati ile ikamilike kabla ya tarehe 30 Machi, isajiliwe, lakini tumeshakubaliana vifaa tiba vitapatikana ndani ya halmashauri kwa sababu tayari wana vifaa ambavyo havitumiki katika vituo vingine, lakini na Serikali itaongezea kuhakikisha kwamba kinaanza kutoa huduma, ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali.

Kituo cha Afya cha Upugi kilikarabatiwa kwa hali ya juu sana na kuletewa mitambo ya kisasa, lakini hela zilipungua kwa kujengea jengo la mashine ya x-ray na ultrasound. Huu mwaka wa nne zile mashine hazijafunga.

Je, lini Serikali itajenga jengo la kuweka mashine ya x-ray na ultrasound katika Kituo cha Upugi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Almas Maige, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ikipeleka fedha katika ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya, kwanza tunapeleka kwa awamu. Awamu ya kwanza, majengo ya OPD, majengo ya maabara ya mama na mtoto; lakini awamu ya pili tunatenga majengo mengine ya Vipimo ya x-ray, ultrasound na wodi, lakini kwa taarifa ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitoa kwamba fedha hazikutosha kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya x-ray na ultrasound, nimhakikishie kwamba Serikali kwa maana ya fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri na Serikali Kuu tutakaa tuone wapi tunapata fedha ili tuweze kukamilisha majengo hayo, ahsante. (Makofi)
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Nakapanya, jengo la upasuaji limekamilika na baadhi ya vifaa vya upasuaji vipo na ambulance ipo.

Je, ni lini Serikali itakamilisha baadhi ya vifaa vya upasuaji ili kituo kile kianze kutoa huduma ya upasuaji na kumsaidia mama na mtoto katika kituo kile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kungu, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya hiki cha Nakapanya ni kweli kwamba kuna baadhi ya vifaa tiba vimeshafika, lakini tayari tumepanga watumishi kwa ajili ya kuanza kutoa huduma na tunafahamu kwamba kuna baadhi ya vifaa tiba hasa kwenye jengo la upasuaji bado havijafika.

Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye bajeti ya mwaka huu, vituo vyote hivi vya afya vilivyokamilika ikiwemo hiki cha Nakapanya kimetengewa fedha kati ya ile shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya kupeleka vifaa tiba ili vianze kutoa huduma za upasuaji kwa wananchi, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA. Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali.

Kwa kuwa miundombinu iliyopo ni chakavu na ina hadhi ya kituo cha afya, Halmashauri ya Wilaya ya Meatu imetenga kiasi cha fedha kwa ajili ya kuanza miundombinu mipya.

Je, Serikali haioni haja ya kujenga miundombinu mipya inayokidhi hadhi ya Wilaya kwa kuwa hospitali hiyo ina eneo la hekari za ziada 17?

Mheshimiwa Spika, hospitali hii ina upungufu mkubwa wa watumishi kwenye eneo la wauguzi wenye degree na wenye weledi; mahitaji ni wauguzi 24 tuliye naye ni mmoja. Je, Serikali haioni haja ya kutuletea wauguzi wenye weledi ukizingatia tumejenga Jengo la ICU? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuwapongeza Halmashauri ya Meatu kwa kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kuendelea na ujenzi na ukarabati wa Hospitali ya Halmashauri ya Meatu, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imefanya tathmini nchini kote hospitali chakavu 50 ambazo zinaupungufu wa Miundombinu zimeanza kutengewa fedha shilingi bilioni 16.5 mwaka huu wa fedha, lakini hospitali 39 ikiwemo ya Meatu zinatengewa fedha kwa mwaka ujao wa fedha. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba kazi ya ujenzi wa Majengo hayo itafanyika.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kwamba Halmashauri ya Meatu ni miongoni mwa Halmasahuri zenye upungufu wa watumishi. Hata hivyo Serikali kwenye mwaka wa fedha uliopita imeajiri jumla ya watumishi wa afya 10,462 na Halmashauri ya Meatu imepata jumla ya watumishi 104 wakiwemo wauguzi, lakini pia na madaktari na zoezi hili tutaendelea kulitekeleza kwa awamu, ahsante sana.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, naomba nimtake Waziri, pamoja na kwamba wataalamu wamefanya mambo haya, lakini Wakuu wa Wilaya walipaswa Kwenda kufanya mkutano pale kwa pande zote mbili na kuonesha beacon, lakini jambo hilo halijafanyika.

Je, uko tayari sasa kuwataka Wakuu wa Wilaya kwa muda maalum kwenda kutekelza agizo hili?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa jimbo langu linapakana pia na Mkoa wa Simiyu na Mkoa wa Manyara na tatizo hili mipaka limekuwa kubwa.

Je, agizo hilo pia utamwagiza pia Mkuu wa Mkoa wa Singida na Mkuu wa Mkoa wa Manyara kwenda kufanya mambo haya haya ili tatizo hili liweze kuisha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki ama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nitoe rai kwa Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya hizi na Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, kama ambavyo maelekezo ya Serikali siku zote yamekuwa yakitolewa kwamba ni muhimu na ni lazima kufika katika maeneo yenye migogoro ya mipaka kati ya kijiji na kijiji, kata na kata lakini kati ya wilaya na wilaya na mkoa na mkoa, ili kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto za mipaka kwa kutumia njia shirikishi na kuhakikisha kwamba wananchi wanaendelea kuishi kwa amani na utulivu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naelekeza Wakuu wa Wilaya hizi na Mikoa ya Manyara lakini na Singida kuhakikisha kwamba wanatekelza haya maelekezo ya Serikali, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, ninaipongeza sana Serikali kwa majibu mazuri haya ambayo yanaleta matumaini kwa wananchi wa Jimbo la Singida Mjini. Nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Kwa kuwa, uwepo wa hospitali ya Wilaya unaenda sambamba na ujenzi wa vituo vya afya. Wananchi wa Kata ya Kisaki wamejenga kituo chao cha afya na Serikali ilileta Shilingi Milioni 50 na kituo hakijakamilika.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukamilisha kituo hicho cha afya?

Swali la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri utakuwa tayari kuambatana nami kwa ajili ya kwenda kutembelea maeneo yote hayo ambayo tumeyataja hapo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima, Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima kwa namna ambavyo anawatendea haki wananchi wa Jimbo la Singida Mjini, nimhakikishie kwamba katika zahanati ile ambayo tayari Serikali ilipeleka shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji katika Kata ya Kisaki, natoa maelekezo ambayo tayari Ofisi ya Rais TAMISEMI tulikwishayatoa kwamba zahanati zote ambazo zilipokea shilingi milioni 50 kama hazijakamilika ni lazima Halmashauri kupitia mapato yao ya ndani watenge fedha na kukamilisha. Kwa hivyo, natoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Singida kuhakikisha zahanati hiyo inakamilishwa.

Mheshimiwa Spika, pili, niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge tutakubaliana baada ya kikao hiki tupange ili twende kufanya ziara katika Jimbo lake. (Makofi)
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa, sasa Hospitali ya Wilaya ya Ngorongoro imeanza kutoa huduma; Je ni lini sasa Serikali itapeleka Wauguzi pamoja na vifaa tiba ambayo ni changamoto kubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zaytun Swai, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Ngorongoro inafanya kazi lakini tunafahamu kwamba bado kuna upungufu wa vifaa tiba na kuna upungufu wa watumishi. Ndiyo maana katika ajira za mwaka huu wa fedha, Serikali inakwenda kuajiri watumishi wa afya 7,600 ambao watapelekwa katika maeneo mbalimbali ikiwepo Hospitali ya Halmashauri ya Ngorongoro lakini pia imetenga fedha kwenye mwaka ujao Shilingi Bilioni 69 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hospitali hii pia itapewa kipaumbele.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa katika Hospitali yetu ya Mkoa wa Manyara tuna jengo moja tu lililokamilika ambayo ni maternity ward. Je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha majengo yote ya hospitali ikiwemo word na jengo la upasuaji na jengo la radiology ili kurahisisha utoaji wa huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Regina Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie kwamba mpango wa Serikali ni kuhakikisha hospitali za Rufaa za Mikoa zote zinakuwa na majengo yote muhimu kwa ajili ya kutoa huduma za afya. Kwa hivyo, hospitali hii ya Mkoa wa Manyara nayo ambayo ina upungufu wa wodi, majengo ya upasuaji na majengo ya radiology tutahakikisha tunaendelea kutafuta fedha ili majengo hayo yajengwe kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, pale kwenye hospitali ya Wilaya ya Makandana tunaishukuru sana Serikali imepeleka vyombo muhimu sana kwa maana ya X-Ray na Ultrasound, lakini pale kuna Mtaalam mmoja kiasi kwamba akiugua au akipata dharura huduma hiyo inasitishwa kwa muda pale.

Je, ni lini Serikali itatuongezea Mtaalam mwingine kwa ajili ya Ultrasound na X-Ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Suma Fyandomo Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Rungwe maarufu Makandana ni muhimu sana inaendelea kutoa huduma za jamii kwa wananchi wa Rungwe, Serikali imetambua uhitaji wa vifaatiba kama X-Ray na Ultrasound imepeleka inafanya kazi. Ni kweli kwamba tuna mtumishi mmoja lakini mpango wa Serikali ni kuhakikisha tunaendelea kuajiri watumishi hao na hivi sasa tumeweka mpango mkakati wa kuwasomesha wataalamu wa usingizi na Radiology ili wawe wa kutosha katika halmashauri zetu. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatafuta watumishi ili kuongeza watumishi katika hospitali ile.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Ningependa kuuliza Serikali, Je, ni lini itapeleka fedha za kukamilisha ujenzi na kununua vifaatiba kwa ajili ya hospitali za Wilaya za Biharamulo, Bukoba DC, Karagwe na Kyerwa ili ziweze kukidhi viwango vya kuwa hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hospitali zetu za Halmashauri zikiwemo hizi za Biharamulo, Bukoba, Kyerwa na maeneo mengine lakini nchini kote tuna upungufu wa baadhi ya vifaatiba na ndiyo maana katika bajeti zetu zote tumeendelea kutenga fedha na bajeti ijayo tumetenga Shilingi Bilioni 69. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutahakikisha tunazipa vipaumbele hospitali hizo.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Tunaendelea kuishukuru Serikali kwa jinsi ambavyo inaendelea kupambana kuongeza vituo vya afya na vifaa kama ilivyojielekeza.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo changamoto kubwa ya watumishi kutokukaa katika vituo vya afya ni ukosefu wa nyumba.

Je, nini mkakati wa Serikali kuwajengea watumishi wa afya nyumba ili waweze kukaa kwenye vituo hivyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dokta Florence Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tuna upungufu wa nyumba za watumishi katika vituo vyetu na mpango wa Serikali sasa ni kuendelea kutenga fedha kupitia mapato ya ndani lakini pia kutoka Serikali Kuu kuhakikisha nyumba za watumishi zinajengwa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mpango huu tayari umeratibiwa.
MHE. JUSTINE L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, ninataka kujua ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba na watumishi katika zahanati za Lugalo, Masege na Mbawi pia katika vituo vya afya vya Ruaha Mbuyuni, Ilula na Mluhe.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justin Nyamoga Mbunge wa Jimbo la Kilolo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyote ambavyo amevitaja ni kipaumbele cha Serikali kuhakikisha vinapelekewa vifaa tiba na watumishi na ndiyo maana tunakwenda kuajiri watumishi 7,600 mwaka huu wa fedha pia tumetenga Shilingi Bilioni 69.95 kwa ajili ya vifaa tiba. Nimhakikishie kwamba tutatoa kipaumbele katika vituo hivyo. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, kuna upungufu mkubwa wa watumishi katika hospitali zetu Wilaya ya Itilima na Wilaya ya Busega. Je, ni lini Serikali italeta watumishi wa kutosha katika Wilaya hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Itilima na Busega ni moja ya Halmashauri zenye upungufu wa watumishi lakini zitapewa kipaumbele kwenye ajira hizi ambazo zimekwishatangazwa. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana Wilaya ya Kishapu ina vituo vya afya vitatu ambavyo vimekamilika na vimeanza kufanyakazi lakini kuna tatizo kubwa la upungufu wa watumishi katika vituo hivyo vya Dulisi, Mwangalanga pamoja na Mwigumbi.

Je, ni lini Serikali italeta watumishi wa kutosha pamoja na tatizo zima la vifaa tiba kushughulikiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Butondo Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli vituo ambavyo amevitaja vina upungufu wa vifaa tiba lakini pia upungufu wa watumishi. Kama ambavyo nimejibu kwenye maswali mengine ya nyongeza na swali la msingi kwamba Serikali imeweka kipaumbele cha kuajiri watumishi na kuwapeleka kwenye vituo hivyo lakini pia kuhakikisha tunanunua vifaa tiba na kupeleka kwenye vituo hivyo. Nimhakikishie Mheshimiwa Butondo kwamba Jimbo lake la Kishapu nalo litapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba katika hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe ikiwepo ultrasound pamoja na x-ray? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Mariki Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ukosefu wa vifaa tiba katika Hospitali ya Halmashauri ya Mpimbwe lakini hospitali zingine za Halmashauri na vituo vya afya ni kipaumbele cha Serikali nimuhakikishe Mheshimiwa Mbunge katika bajeti hii inayokuja lakini watumishi ambao wanaajiriwa katika mwaka huu wa fedha tutakipa kipaumbele kituo hiki cha afya na Hospitali ya Halmashauri ya Mpimbwe. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Na mimi naomba kuuliza katika Mkoa wetu wa Pwani katika Wilaya ya Kibiti tuna hospitali ya Mbochi na Mwambao ambayo imekamilika. Ni lini Serikali mtaleta vifaa tiba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alice Kaijage Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye vifaa ambavyo vitakwenda kununuliwa kwenye mwaka wa fedha ujao tutatoa kipaumbele katika hospitali hii ambayo inahitaji vifaa tiba. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Hospitali ya Wilaya ya Kyerwa haina watumishi na hivyo kupelekea wagonjwa wengi kujazana kwenye kituo cha afya cha Nkwenda. Sasa nataka kujua ni lini na ni kwa kipaumbele kiwango gani hiyo hospitali itapewa ili kupunguza adha ambayo kituo cha afya cha Nkwenda inapitia kuwa na wagonjwa wengi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Theonest Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya Kyerwa ina upungufu wa watumishi pamoja na vituo vingine vya afya, lakini nimpongeze Mheshimiwa Mbunge ambavyo ameendelea kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kyerwa ambaye mara kwa mara amekuwa anakumbushia kuhusiana na watumishi katika eneo hilo nimhakikishie kwamba tutaipa kipaumbele cha watumishi hospitali ya Wilaya ya Kyerwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Kwanza nianze kwa kuishukuru Serikali kwa sababu imetupatia fedha zaidi ya Shilingi Milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa wodi za upasuaji pamoja na wodi za akina mama katika kituo cha afya cha Itaka.

Je, Serikali sasa inatuhakikishieje kwamba ujenzi huu utakapokamilika watatupatia Daktari wa upasuaji ikizingatiwa kwamba mpaka sasa hatuna Daktari wa upasuaji lakini kituo kile cha afya cha Itaga kinahudumia Kata takribani Tano kwa maana ya Kata ya Harungu pamoja na Nambizo. Kwa hiyo nilitaka kufahamu commitment ya Serikali kwamba itatuletea lini Daktari wa upasuaji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili mamlaka ya Mji mdogo wa Mlowo una wakazi takribani 100,000 lakini katika hali ya kusikitisha mpaka sasa hivi hatuna Kituo cha Afya pale na sasa hivi ninavyoongea tayari wananchi wamefyatua tofali zaidi ya 150,000 vilevile mamlaka ya Mji imetoa eneo heka kumi…

SPIKA: Mheshimiwa Juliana Shonza uliza swali.

MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, naomba kufahamu sasa ni lini Serikali itatuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Mlowo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Juliana Daniel Sh onza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Shonza kwa namna ambavyo anawasemea wananchi wa Mkoa wa Songwe pia kwa namna ambavyo anaendelea kuwapa ushirikiano Waheshimiwa Wabunge wa Mkoa wa Songwe akiwepo Mheshimiwa Mwenisongole Mbunge wa Jimbo la Mbozi.

Mheshimiwa Spika, Serikali imepeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji katika Kituo cha Afya cha Itaka na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya jengo lile kukamilika tutapeleka Daktari ambaye atatoa huduma za upasuaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na Kata ya Mlowo kuwa na wananchi wengi na haina kituo cha afya nina imani kwamba Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo aliwasilisha vipaumbele vya Kata Tatu za kimkakati nasi tutakwenda kufanya tathmini na kuona kama Mlowo iko katika orodha hiyo basi tutatafuta fedha ili tuweze kujenga kituo cha afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante, napenda kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Simiyu tuna Wilaya Tatu ambazo zina upungufu wa watumishi wa afya. Wilaya ya Meatu, Bariadi na Maswa.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika Halmashauri hizi za Mkoa wa Simiyu kuna upungufu wa watumishi kama ilivyo kwenye Halmashauri nyingine zote hapa nchini, mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi kwa awamu na ndiyo maana ajira 7,612 zimetangazwa na Halmashauri hizi pia zitapewa kipaumbele katika kuwapelekea watumishi hao. (Makofi)
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri katika Kata ya Nanyara pale Songwe pana kituo cha afya ambacho kimejengwa takribani zaidi ya miaka minne sasa na hakina wafanyakazi kabisa wa kutosha.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inapeleka wafanyakazi katika kituo hicho cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga Mbunge wa Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kituo hiki cha Nanyara ambacho kimekamilika zaidi ya miaka Minne iliyopita kina watumishi wachache, nimhakikishie kwamba mpango ni kuhakikisha tunapeleka watumishi ambao angalau watakidhi mahitaji ya kituo cha afya na hivyo tutahakikisha tunapeleka watumishi katika kituo hiki ili waweze kutoa huduma bora za afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii.

Katika Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga mpaka sasa tuna uhaba wa watumishi wa kada ya afya 660. Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta watumishi katika kada hii ya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deus Sangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kipaumbele cha Serikali kwenye vituo vyote vya afya vilivyokamilika vinavyotoa huduma na ambavyo vinatarajiwa kuanza kutoa huduma ni kupeleka watumishi ili viweze kutoa huduma. Ndiyo maana kuna ajira ambazo zimetangazwa. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mkakati wa Serikali ni kuhakikisha watumishi wanakwenda kwenye kituo hicho pia na tutahakikisha watumishi wanakwenda kutoa huduma za afya pale. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika Wilaya ya Kishapu, vituo vya afya vya Mwahalanga, Dulisi na Kishapu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu katika majibu yangu ya awali kwamba mkakati wa Serikali ni kuendelea kuajiri, vituo hivi vya afya ambavyo vina upungufu wa watumishi vitapelekewa watumishi kwenye ajira hii pia kwenye ajira zinazofuata. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na mimi kunipa nafasi niulize swali la nyongeza nalo liko hivi.

Mheshimiwa Spika, baada ya wafadhili waliokuwa wanaendesha kituo cha afya Momela kujiondoa watumishi pia ambao walikuwa wanalipwa na wale wafadhili Afrika waliondoka. Sasa hivi huduma zimedorora; Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka watumishi na wataalam kwa ajili ya kufanya huduma zikae vizuri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dokta Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kuna upungufu wa watumishi katika kituo hicho cha afya na nimhakikishie kwamba tutaendelea kupeleka watumishi pale ili waendelee kutoa huduma za afya na tutaangalia katika ajira hizi na zinazofuata ili tuhakikishe kwamba kituo kile kinatoa huduma bora kwa wananchi.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Halmashauri ya Kyerwa ina vituo vya afya Vitatu licha ya kuwa na wakazi zaidi ya 600,000. Napenda kujua tayari kituo cha afya cha Kamuli kimekamilika changamoto imekuwa vifaatiba na Madaktari.

Ni lini madaktari watapelekwa ili hicho kituo kiweze kuongezeka na kusaidia kupunguza adha kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyote ambavyo vimekamilika na ndio maana jana wakati tunapitisha bajeti hapa tunashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kupitisha bajeti ya Wizara hii ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo kwa kiasi kikubwa kwenye sekta ya afya tumeweka ununuzi wa vifaatiba pia na ajira za watumishi.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika kituo hiki cha afya katika Halmashauri ya Kyerwa pia tutahakikisha kinapata vifaatiba na watumishi ili kianze kutoa huduma bora zaidi za afya kwa wananchi. (Makofi)
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali ina mpango gani wa kupeleka watumishi katika kituo cha afya Lukuledi ambacho kinakamilika ambacho kitahudumia Kata zaidi ya Tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Agnes Hokororo Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kituo cha afya hiki cha Lukuledi ambacho amekitaja Mheshimiwa Mbunge ni miongoni mwa vituo ambavyo vitapelekewa watumishi ili viendelee kutoa huduma bora za afya. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakipa kipaumbele kituo cha afya hiki?
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Kipo Kituo cha afya Rungwa ambacho tunaendelea na ujenzi na hakijasajiliwa kama kituo cha afya na watumishi ni wa zahanati. Je, sasa Serikali iko tayari kupeleka watumishi kwa Kituo hiki cha Afya cha Rungwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahaya Massare, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kituo hiki cha afya ambacho kinaendelea na ujenzi baada ya kukamilika tutafanya mpango wa kuhakikisha kwamba tunapeleka watumishi ili kianze kutoa huduma za afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Jiografia ya Jimbo la Kyerwa ni milima na mabonde, hivyo kuhitaji madaraja na barabara kwa maana maeneo mengi hayapitiki. Bajeti ya bilioni mbili haitoshi, nataka kujua commitment ya Serikali ni kwa kiwango gani itaongeza bajeti ili kuweza kusababisha maeneo mengi yafikike?

Mheshimiwa Spika, swali la pili barabara ya Nkwenda- Kakanza-Kimuli mpaka Mabira inatumika na kata zaidi ya 5 na kwa TARURA wamepewa scope ya kilometa tatu ambayo ina urefu wa zaidi ya kilometa 30. Je, ni sahihi kweli kutoa kiwango hiki cha fedha kwa barabara hii nataka kujua mkakati wa dharura kupeleka fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anatropia Lwehikira Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kumpongeza Mheshimiwa Anatropia kwa namna ambavyo anashirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kyerwa Mheshimiwa Innocent Bilakwate na hoja hizi zote ambazo Mheshimiwa Mbunge amezileta Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo amekuwa mara kwa mara anazileta, kwa hiyo niwapongeze kwa ushirikiano huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na fedha kwa maana za madaraja, hali ya milima na mabonde na hali ya mvua tunafahamu na ndio maana Serikali imeendelea kuongeza fedha kutoka bilioni moja mpaka bilioni mbili na milioni mia nane na tisini katika Wilaya ya Kyerwa ili kuhakikisha inaendelea kujenga madaraja, makalveti na barabara. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Serikali itaendelea kuweka jitihada hizo.

Mheshimiwa Spika, hii barabara ambayo inahudumia kata nyingi na inahitaji fedha zaidi ndio maana Serikali imeongeza bajeti na tutaendelea kuongeza bajeti ili tuhakikishe tunafikia kilometa zote 30 ili kata zote ziweze kunufaika. Ahsante sana.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Barabara za Wilaya ya Ileje zinakabiliwa na changamoto kubwa sana ya kutopitika hasa wakati wa masika. Naomba kufahamu ni lini Serikali itaipatia fedha TARURA Wilaya ya Ileje ili kuwaondolea adha wananchi wa Wilaya ya Ileje? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka huu wa fedha, moja ya halmashauri ambazo zimeongezewa bajeti ili kuweza kukidhi matengenezo ya barabara za vijijini na mijini ni Halmashauri ya Wilaya ya Ileje. Hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, hiyo barabara ambayo ameitaja ni sehemu ya bajeti ya mwaka ujao wa fedha na tutahakikisha kwamba tunaendelea kuitengeneza kwa awamu ili iweze kupitika vizuri. Ahsante.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na Serikali kuongeza bajeti kwa Wilaya ya Kyerwa, lakini tulileta ombi maalum kwa ajili ya barabara ya Kibingo kwenda Rwesinga, Barabara ya Mabira kwenda Nyamiri- Makamuri, barabara ya Kikukuru -Mkunyu - Lwele, barabara ya Kakanya - Lwele pamoja Bushongore. Ombi hili ni lini litatekelezwa ili kuondoa changamoto iliyopo Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Bilakwate kwa namna ambavyo anaendelea kuwapambania wananchi wa Jimbo la Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, pia nimhakikishie ni kweli ameleta maombi maalum ya barabara zenye urefu wa takribani kilomita 55 ambazo amezitaja. Tayari Ofisi ya Rais, TAMISEMi tumepokea na tutaanza utekelezaji mwaka ujao wa fedha kuhakikisha barabara zote zinapitika vizuri. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Je, ni kwa nini Serikali isipeleke pesa za miradi hii ya TARURA kwa meneja wa wilaya badala ya mkoa ambako mara nyingi zimekuwa zinasababisha urasimu kwenye utekelezaji wa miradi hii ya barabara zilizo chini ya TARURA?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba fedha za matengenezo ya barabara zimekuwa zikipelekwa katika ngazi ya mikoa na siyo ngazi ya Mameneja wa Wilaya na sababu ya msingi ilikuwa muundo wa TARURA uliweka watendaji wengi zaidi kwenye ngazi ya mkoa kwa maana ya wataalam; Wahasibu, wataalam wa manunuzi na wengine. Kwa hiyo ilikuwa ni vyema sana kupeleka fedha kwenye ngazi ya mkoa ambayo ina watendaji wengi kuliko halmashauri. Utaratibu huu tunaendelea kuutekeleza, lakini pale tutakapoona tuna sababu ya kupitia upya tutafanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Barabara ya Katesi - Iteka inaunganishwa na daraja muhimu katika Mto Mpanda, kwa bahati mbaya daraja hilo limekatika. Je, ni lini Serikali itaongezea fedha TARURA ili walitengeneze daraja hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sebastian Kapufi, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda pia ni moja ya halmashauri ambazo zimeongezewa bajeti ya barabara. Lakini nimhakikishie kwamba mpango wa Serikali ni kuainisha na tayari nimeshainisha madaraja korofi yote na makalvati ili kuhakikisha tunaongeza fedha za ujenzi wa madaraja hayo yaweze kupitika. Hivyo nawaelekeza TARURA, Mkoa wa Katavi na Manispaa ya Mpanda wahakikishe wanaleta andiko la daraja hili ili TAMISEMI tuweze kuona namna ya kutafuta fedha kwenda kufanya ujenzi wa daraja hilo. Ahsante.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Kibiti tumepatiwa fedha shilingi bilioni 6.2, tumejenga daraja zuri sana pale Mbochi ambalo linaunganisha wananchi wa Mbwela na Mbochi na kuja Kibiti Mjini. Hata hivyo, kuna kipande cha kilometa 35 ambacho ikinyesha mvua kinakuwa kipo katika hali mbaya sana.

Je, ni nini tamko la Serikali ili kuweza kuhakikisha kwamba tunakwenda kutengeneza kipande kilichobaki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Twaha Mpembenwe, Mbunge wa Jimbo la Kibiti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na tuendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi sana ambazo amezileta katika majimbo yetu ikiwepo Jimbo la Kibiti. Nimhakikishie kipande cha kilomita tatu ni kipaumbele kwa sababu kama tumepeleka billions za fedha katika daraja lazima tukamilishe kilomita tatu ili hilo daraja liweze kuwa na tija. Kwa hiyo namhakikishia kwamba tutatafuta fedha kuhakikisha kilomita hizi tatu zinatengenezwa ahsante.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipatia fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza. Mazingira ya Kyerwa na Muleba yanafanana kutokana na mvua nyingi, milima na mabonde. Tuna barabara nyingi ambazo hazipitiki hasa kipindi cha mvua. Tulileta ombi letu kwa ajili ya barabara ya Kimea Burigi na Luhanga- Kiholele. Je, ni lini Serikali itatupatia pesa kwa ajili ya kutengeneza hizo barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oscar Kikoyo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba jimbo hili pia lina changamoto ya milima, mabonde na linahitaji kupata fedha za kutosha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hizi na ni kweli kwamba Mheshimiwa Mbunge alileta ombi maalum. Nimhakikishie kwamba maombi maalum yote yaliyoletwa yanafanyiwa tathmini na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia TARURA na tutahakikisha yanatafutiwa fedha ili yaweze kufanyiwa kazi. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge nimhakikishie kwamba tutalipa kipaumbele pia eneo ambalo wameomba maombi maalum. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, nina swali moja tu la nyongeza. Kwa kuwa kumekuwepo na maeneo mengi hapa nchini yaliyokosa sifa ya kuwa hifadhi na yamekuwa na migogoro mikubwa sana na wananchi. Ni lini Serikali sasa itafanya tathmini ya maeneo yote haya na kuyaleta hapa ili tuyagawe kwa wananchi, yote yaliyokosa sifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na maeneo mengi ambayo yamekuwa hifadhi kwa muda mrefu, lakini baadhi ya maeneo yamekuwa na changamoto ya migogoro kati ya wananchi pia na mamlaka za hifadhi.

Nimhakikishie kwamba Serikali inatambua changamoto katika maeneo hayo na tathmini inafanyika kwa kuzingatia sheria, taratibu na miongozo ya maeneo ya hifadhi ili kuhakikisha yale ambayo yanaendelea kukidhi sifa za kuwa maeneo ya hifadhi yaendelee kuwa maeneo ya hifadhi lakini yale ambayo yamepoteza sifa, Serikali inachukua hatua za kuendelea kuwapatia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili tunalifanyia kazi ikiwemo la msitu huu ambao tumeujibia. Ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Napenda kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba kwa mfano sisi pale katika Mkoa wa Simiyu tuna Pori la Maswa na ni pori kubwa na ni maarufu. Je, Serikali ina mkakati gani wa kutangaza mapori haya kimataifa ili yaweze kutumika kwa maana ya kukaribisha watalii, vilevile kuhakikisha kwamba wananchi wa maeneo haya wananeemeka na mapori haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stanslaus Nyongo, Mbunge wa Jimbo la Maswa Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli katika Halmashauri ya Maswa na Mkoa wa Simiyu kuna Pori maarufu la Maswa na kwamba Serikali imekuwa na mkakati wa kuhakikisha kwamba inatangaza mapori haya ili watalii waendelee kuja na Serikali yetu iendelee kupata mapato. Ndio maana hivi sasa tunaongea Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan anaendelea kuitangaza Royal Tour ili tuhakikishe watalii zaidi wanaendelea kuongezeka katika hifadhi zetu lakini maeneo ya kitalii ikiwepo Pori la Maswa. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba mpango wa Serikali ni huo na utahakikisha kwamba wananchi wanaoishi maeneo ya jirani pia wananufaika na mpango huo, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri na ya kuridhisha ya Serikali ningeomba kuuliza haya maswali mawili. Moja, stendi yetu ya Magufuli inaruhusu kuingiza mabasi yote yanayotoka mikoani bila kwenda kokote na kushusha pale abiria, lakini pamekuwepo bado na mabasi mengi kwenda Urafiki na maeneo ya pale kwa Wachina na Maghorofani. Pamoja na maelekezo mengi yanayotolewa na viongozi wa mkoa na wilaya. Je, Serikali inatoa kauli gani juu ya kushindwa kwa muda mrefu kusimamia maelekezo yake?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, ni ukweli stendi ile pamoja inaenda kukamilika kwa wachache walioingia kupitia mnada wanalipa square mita au mita za mraba Sh.40,000 tofauti na maeneo mengine ya Jiji la Dar es Salaam ikiwepo hata maeneo ya pale Mlimani City, kati ya shilingi 15,000 hadi shilingi 25,000, lakini hawa wanalipa shilingi 40,000.

Je, Serikali haioni sasa ni sababu ya kupunguza kufikia hiyo kati ya shilingi 15,000 hadi shilingi 25,000 ili matumizi yaende kama yalivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Mtemvu kwa kazi kubwa anayoifanya kuwasemea wananchi wa Jimbo la Kibamba na nimwakikishie Serikali itaendelea kumpa ushirikiano ili aweze kutekeleza miradi mbalimbali ya wananchi wa Kibamba. Kuhusu mabasi ambayo hayaingii kwenye stendi ya Magufuli, ni kweli kumekuwa na baadhi ya makampuni ambayo hayatumii ipasavyo stendi kadri ya maelekezo na malengo ya ujenzi wa stendi ile. Kwa hivyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tunalichukua hili tunalifanyia kazi na tutatoa maelekezo mahususi kuhusiana na utaratibu wa mabasi kutumia stendi ile ya Magufuli.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na gharama ya upangishaji kwa square mita kufika hadi Sh.40,000 mapendekezo yake ni Sh.15,000 hadi Sh.25,000 naomba niseme tunalichukua hilo kama Serikali tutalitazama na tuweze kuona mazingira kama yanaruhusu basi tuweze ku- review bei hizo ili wananchi wapate unafuu katika upangishaji.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Mkoa wa Songwe ni miongoni mwa mikoa mipya na mpaka sasa hatuna stendi ya mkoa, tayari fedha zilishatengwa. Naomba kufahamu nini mkakati wa Serikali katika kutupatia hizo fedha bilioni 29 ili tuweze kujenga stendi ya mkoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mkoa wa Songwe kwa sababu ni mpya hauna stendi ya mabasi ya mkoa na kama alivyosema Mbunge Serikali tayari imeshaweka mpango wa kujenga stendi ya mabasi ya Mkoa wa Songwe na imeshatenga fedha. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba kazi iliyopo sasa tunatafuta fedha ili twende kujenga stendi ya kisasa ya Mkoa wa Songwe.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa stendi ya Mbezi ni miongoni mwa miradi ya kimkakati inayosimamiwa na TAMISEMI. Je, ni lini mradi wa kimkakati wa Soko la Mlandizi utajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya maeneo yote ambayo yanahitaji kujengewa stendi za kimkakati ikiwepo Halmashauri ya Kibaha. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tushaelekeza halmashauri walete andiko walishaleta na najua kulikuwa kuna mazungumzo ya eneo wapi tujenge ile stendi. Nikuhakikishie kwamba TAMISEMI tunaendelea na kufanya tathmini ya mapendekezo ya halmashauri ili twende kujenga stendi ile na tutafanya hivyo mapema iwezekanavyo. Ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Naomba kuuliza kwa kuwa akinamama wa Mkoa wa Dar es Salaam wengi ni akinamama lishe na wanafanya shughuli ndogondogo, lakini katika eneo hilo hilo la stendi ya Mbezi bado kuna eneo kubwa ambalo Serikali inaweza ikawajengea vibanda vidogo vidogo. Je, Serikali haioni haja hata kwa kutumia Mfuko wa Akinamama ile asilimia yao kuwajengea mabanda rahisi ya kuweza kufanya kazi zao, akinamama wote wa Mkoa wa Dar es Salaam? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunahitaji kuboresha maeneo ya wafanyabiashara wadogowadogo na ndio maana Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan ameelekeza kuboresha maeneo ya wafanyabiashara wadogo wadogo wakiwemo akinamama ntilie lakini pia machinga na wafanyabiashara wengine. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo la Mbezi ambalo anasema lina nafasi ya kujenga tutakwenda kulitazama ili tuone uwezekano wa kuwekeza hapo. Wazo lake la kutumia asilimia 10 pia tutalifanyia tathmini kuona au kutafuta chanzo kingine kwa ajili ya ujenzi huo. Ahsante.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu ya kutia matumaini ya Serikali awali ya yote kwanza nitoe pole kwa wananchi wa Jimbo la Singida Kaskazini kufatia ajali mbaya iliyotokea juzi na kuuwa wananchi wanne hapo hapo na majeruhi 20 lakini hawakuweza kupatiwa matibabu kwa wakati na ipasavyo kwa sababu ya kukosa vifaa tiba katika hospitali zetu. Lakini...

SPIKA: Mheshimiwa Mbunge ngoja tuelewane vizuri, kwanza ni kipindi cha maswali, pili unaongeza hoja hapo kwamba hawakupatiwa matibabu, hiyo ni hoja nzito sana, unao ushahidi ama huna? Kama huna hebu jielekeze kwenye maswali ondoa hiyo habari nyingine kabisa, kwa sababu tusije tukahama kwenye maswali tukaelekea kuanza kushughulika na hiyo hoja kwamba walifariki kwa sababu hawajapatiwa matibabu, hiyo ni hoja nzito sana kuletwa hapa Bungeni.

MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, maswali yangu mawili madogo ya nyongeza. Kwanza, ni lini tutapatiwa ambulance katika hospitali hizi ili kurahisisha huduma kwa wananchi wetu wanaopata magonjwa mbalimbali na mengine ya ghafla kama ajali?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni lini sasa Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika vituo hivi vya afya pamoja na hospitali ya wilaya ili waweze kutoa huduma kwa wakati na ipasavyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abeid Ramadhani Ighondo, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na suala la ambulance katika bajeti inayokwisha mwaka huu tarehe 30 Juni, Serikali imetenga magari ya wagojwa 195 na kila halmashauri itapata gari la wagonjwa ikiwepo halmashauri ya Singida ambayo tutapeleka kwenye hospitali hii. Kwa hiyo nimhakikishie kwamba suala hilo tayari linafanyiwa kazi na gari ya wagonjwa itapelekwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na watumishi ni kweli tuna upungufu wa utumishi, lakini Serikali imetoa kibali tayari hivi sasa vijana wanaendelea kuomba ajira ya watumishi wa kada mbalimbali za afya 7,612 na miongoni mwa watumishi hao watapelekwa katika Wilaya ya Singida.
MHE. SUBIRA K. MGALU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imeleta milioni 500 kumalizia ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ya Kibiti, Kibaha Mjini, Kibaha Vijjini na bilioni moja Halmashauri ya Chalinze. Je, Serikali inatoa ahadi gani kwa wananchi wa maeneo hayo juu ya kuleta vifaa tiba kwa wakati ili iendane na jitihada hizi za uwekezaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Subira Mgalu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa kutambua umuhimu wa huduma za afya kwa wananchi wa Kibiti na wananchi wa Chalinze imepelekwa jumla ya shilingi bilioni moja na milioni mia tano kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya na hospitali. Hata hivyo, nimhakikishie mara baada ya kukamilika kwa vituo hivi Serikali itapeleka vifaa tiba kwa sababu katika bajeti ya mwaka ujao shilingi bilioni 69.95 imetengwa kwa ajili hiyo.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba na watumishi katika zahanati ya Mwashilalage katika Jimbo la Sumve ambayo ujenzi wake umeshakamilika kwa muda sasa na mahitaji ya watumishi na vifaa tiba ni ya hali ya juu kutokana na kwamba kata nzima ya Sumve haina zahanati yoyote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasalali Mageni, Mbunge wa Jimbo la Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na vifaa tiba na watumishi vyote viko kwenye mpango na viko tayari. Watumishi wanaendelea kuajiriwa hivi sasa na matarajio ya Serikali ifikapo Julai, watumishi watapelekwa kwenye vituo vyetu na tutahakikisha tunatoa kipaumbele kwenye zahanati ambayo Mheshimiwa Mageni Kasalali ameongelea.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na vifaa tiba mwaka ujao wa fedha tumetenga 69.95 bilioni kwa ajili ya vifaa tiba na tutahakikisha pia vinapelekwa kwenye zahanati hiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Kituo cha Afya cha Chalangwa kimekamilika muda mrefu pamoja na jengo la Mochwari limekamilika, lakini mpaka sasa hivi hakuna majokofu wala vifaa tiba: Je, Serikali inatuahidi nini kupeleka vifaa tiba hivi pamoja na jokofu kwenye Kituo cha Afya cha Chalangwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masache Kasaka Mbunge wa Jimbo la Lupa kama ifuatavyo: -

Ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Chalangwa kimekamilika na ni miongoni mwa vituo afya ambavyo vimetengewa fedha ya vifaa tiba mwaka ujao 2022/2023 ikiwemo jokofu kwa ajili ya chumba cha kuhifadhia maiti.
MHE. ATHUMANI A. MAIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza. Katika kituo hicho pia kuna mtambo mkubwa wa kufua nguo ambao screen yake au kisomeo kiliharibika wakati mtambo unapelekwa kwenye site: Je, Serikali iko tayari kuleta spare nyingine ili kituo kile kiweze kufanya kazi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika kituo kile pia kuna mtambo mkubwa wa X-Ray ambao haufanyi kazi kwa sababu hakuna jengo la kufunga mtambo ule: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kusafiri na mimi kwenda huko Upuge ili tukaone ufumbuzi wa kupata jengo jipya la kufunga mionzi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mtambo wa kufua nguo ambao umeharibika naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tutafanya tathmini ya mahitaji kwa maana ya gharama, lakini tutaona kati ya fedha ya mapato ya ndani na kutoka Serikali Kuu ipi inaweza ikatumika kuhakikisha mtambo huo unafanya kazi au tunanunua mtambo mwingine.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Jengo la X-Ray, kwamba X-Ray ipo lakini hakuna jengo, naomba tulichukue suala hili tukalitazame. Pia nitoe wito kwa Halmashauri ya Tabora kuanza kuona uwezekano wa kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kujenga jengo la X-Ray, kwa sababu tayari kuna mtambo na wana mapato ya ndani, wanaweza wakatenga kwa awamu kujenga jengo hilo ili tuweze kutoa huduma hiyo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo niko tayari kuongozana na Mheshimiwa Mbunge tukapitie eneo hilo. Ahsante.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii. Nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini pamoja na majibu hayo, kuna vituo vya afya ambavyo viko mbali sana na Hospitali ya Wilaya kiasi ambacho inakuwa shida kwa wagonjwa kupelekwa katika hospitali hiyo. Kwa mfano, Kituo cha Mtambaswala ni kilomita 70 kutoka Hospitali ya Wilaya, Kituo cha Nanyumbu kilomita 40, Kituo cha Michiga kilomita 30; kwa hiyo, kwa umbali huo, naomba kupata commitment ya Serikali kwa sababu kama tutagawa equally kwa Halmashauri zote, kuna vituo vya afya ambavyo vitakuwa havifanyiwi kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, naomba pia kupata majibu ya Serikali: Ni lini Kituo cha Afya cha Mkwedu ambacho kipo katika Jimbo la Newala Vijijini kitapelekewa gari kwa ajili ya wagonjwa kwa sababu kituo kile kinahudumia kata zaidi ya tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Maimuna Mtanda, Mbunge wa Jimbo la Newala Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Vituo vya Afya vya Mtambaswala, Nanyumbu viko mbali sana kutoka Hospitali ya Halmashauri na Serikali inatambua kwamba vituo vya mbali sana vinahitaji kupata magari ya wagonjwa. Ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha Mheshimiwa Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametupa fedha TAMISEMI kwa ajili ya kununua magari 407. Magari ya wagonjwa 195 kwa kila halmashauri na halmashauri hii ya Nanyumbu itapata na magari 212 kwa ajili ya usimamizi wa huduma za afya katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, utaona tutakuwa na magari zaidi ya hayo, lakini tutaendelea kutoa kipaumbele kwenye vituo vya mbali zaidi ili vipate magari yakiwemo vituo hivi vya afya.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mkwedu, naomba nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatafuta fedha ili tuweze kupeleka gari la wagonjwa. Nafahamu kituo hiki kiko mbali sana na kinahudumia wananchi wengi. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Jimbo la Njombe limekuwa na vituo vitatu vimekamilika muda mrefu sana; na huu mgao wa equal unatupa wasiwasi kwa vile vituo ambavyo vinangojea magari na vimeahidiwa miaka zaidi minne: Je, Serikali itatusaidia kwenye hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunahitaji vituo vyetu viwe na magari ya wagonjwa kila kituo kiwe na gari la wagonjwa. Safari ni hatua. Kwa sasa tunaanza na vituo vile vya kimkakati, lakini mara nyingi uzoefu unaonesha vituo vya afya vingine vinaweza vikawa saved na magari ya wagonjwa yaliyo katika Hospitali za Halmashauri au katika vituo vya afya vya jirani. Kwa hiyo, tutaendelea kuangalia umbali wa kituo cha afya kutoka hospitali na pia population ambayo ina- save ili kuhakikisha kwamba tunapeleka magari katika vituo hivyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Geita ina majimbo mawili na hospitali mbili za wilaya. Sasa kwa maelezo ya Waziri, ina maana likija gari moja itakuwa ni ugomvi ikakae hospitali gani; aidha, likae Jimbo la Geita Vijijini au Busanda, ambapo kila jimbo lina hospitali: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa special kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Geita kuleta magari mawili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, magari ya wagonjwa yatakayonunuliwa ni magari 195, nasi tuna Halmashauri 184. Kwa hiyo, utaona tuna magari 11 ya ziada na tutaangalia mazingira ambayo tuna ulazima wa kuongeza gari kwenye Halmashauri, tutaongeza. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya tathmini kuona magari yaliyopo Geita Vijijini na Mjini na uhitaji na hivyo tunaweza kufanya maamuzi. Kwa hiyo, tutafanya hivyo kwa kadri ya mazingira. Ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itajenga vyumba vya kuhifadhia maiti katika Vituo vya Afya vya Nzihi pamoja na Kiponzero? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilishatoa maelekezo ya Halmashauri zote kuanza kwa kutumia mapato ya ndani kwa ujenzi wa miundombinu ambayo iko ndani ya uwezo wao ikiwemo majengo ya kuhifadhia miili ya marehemu kwa maana ya mochwari. Kwa hiyo, naomba Halmashauri ya Wilaya ya Iringa iangalie uwezekano wa kuanza ujenzi wa mochwari kwenye vituo vya afya vya Nzihi na Kiponzero. Pia Serikali tukipata fedha, tutaunga mkono juhudi hizo za Halmashauri. Ahsante. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Halmashauri ya Wilaya ya Same ina majimbo mawili ambayo moja ni la Mashariki na Magharibi na yako mbalimbali sana; lakini Hospitali ya Wilaya iko upande mmoja tu wa magharibi na hata kituo cha afya kilichoko mashariki hakina gari la wagonjwa. Mheshimiwa Waziri, naomba hili aliangalie na aniambie atafanya nini hapa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya vituo vya afya viko mbali sana kutoka Hospitali za Halmashauri ziliko ikiwemo kituo hiki cha afya ambacho Mheshimiwa Mbunge amekitaja. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya tathmini na kuona uwezekano wa kupata gari la wagonjwa kwa ajili ya kituo hiki cha afya ili kuweza kusogeza huduma kwa wananchi.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba mpaka sasa haina gari hata moja la uhakika la wagonjwa; na ni Halmashari ya Wilaya ambayo imeundwa na majimbo mawili; Jimbo la Kwimba na la Sumve. Mpaka sasa kwenye Jimbo la Sumve hakuna kabisa ambulance: Mheshimiwa Waziri huoni kwamba umefika wakati wa Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba yenye majimbo mawili na Halmashauri zote zenye majimbo mawili kugawiwa ambulance kwa kuzingatia kwamba kila Jimbo lipate ambulance yake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasalali Mageni Mbunge wa Jimbo la Sumve, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nipokee taarifa ya Halmashauri hii ya Kwimba kwamba haina gari la uhakika hata moja la wagonjwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wananchi wetu wanapata uhakika wa huduma za rufaa na dharura. Kwa hiyo, tutahakikisha tunapata gari kwa ajili ya Halmashauri ya Wilaya ya Kwimba.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kugawa magari mawili kwenye Halmashauri zenye majimbo mawili, tutafanya tathmini kulingana na uhitaji kwa kadri ya vigezo vya kitaalamu na tutaona, ziko Halmashauri zitapata magari zaidi ya moja na pia ziko Halmashauri ambazo zinaweza zikapata gari moja. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Serikali ambayo sisi kule mkoani katika hatua ya RCC tulikaa, sasa sijui yalikwamia wapi? Nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa mchakato huu huwa unaandaliwa na wataalamu na ambao wako chini ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Je, kama alivyoeleza kwamba hawajapokea wasilisho, hawaoni tu kwamba Mkoa wa Tanga ndiyo mkoa pekee nchini ambao una wilaya nane na una Majimbo ya Uchaguzi 12 na Halmashauri 11? Sasa ni lini Serikali yenyewe tu itaweza kufanya maamuzi ya kuugawa mkoa huu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tunaposema utawala bora ni pamoja na upelekaji wa huduma kwa wananchi. Sasa wataalamu hawa katika ngazi za elimu na afya wanapata taabu kubwa sana kwa sababu wanatumikia eneo kubwa la kiutawala: Ni lini sasa Serikali itatenda kama inavyosema kuhusu eneo zima la utawala bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunafahamu Mkoa wa Tanga ni miongoni mwa mikoa yenye Halmashauri nyingi na ni mkoa mkubwa na maana yake kunakuwa na changamoto za aina yake katika uendeshaji. Ila kwa mujibu wa sheria, uanzishaji ni lazima uanzie ngazi ya mkoa wenyewe kama ambavyo sheria hii inaelekeza. Kwa hiyo, pamoja na kwamba Serikali kwa maana ya Serikali Kuu inaona, lakini wajibu wa Halmashauri, mkoa wenyewe, na vijiji utekelezwe ili tuweze kuanzisha mkoa huu kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na changamoto ya ukubwa wa mkoa ambao unapelekea wataalamu wa afya na elimu kushindwa kutekeleza majukumu yao ya utawala bora, tunaendelea kuwezesha kwa kadri ya ukubwa wa mkoa kwa maana ya miundombinu, usafiri na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi ni kuleta hoja hiyo ili Serikali iweze kuchukua maamuzi stahiki. Ahsante.
MHE. DUNSTAN KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; naomba niulize swali moja la nyongeza. Ugawaji wa Mkoa wa Tanga ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano alipokuja kwenye Mkoa wa Tanga, na hii ilikuwa ni baada ya Wabunge wa Mkoa wa Tanga kumuomba kwamba jambo hili tumeshalijadili kwenye RCC.

Je, hata baada ya ahadi ya Mheshimiwa Rais bado tunatakiwa jambo hili tena kulijadili kwenye mkoa kwa mara nyingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dunstan Kitandula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kadri ya majibu yangu ya jibu la msingi, kwamba kuna taratibu ambazo zipo kwa mujibu wa sheria, na Mheshimiwa Rais alitoa ahadi hiyo, na sisi ahadi hiyo na sisi ahadi za viongozi wetu, Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Makamu Rais, Waziri ni maelekezo ni maelekezo tutafanya kazi hiyo. Hata hivyo niwaombe tufuate utaratibu ule kwa kadri sheria ilivyo.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Waziri ni lini Serikali itakamilisha mpango wa kupanua Mji wa Moshi na hatimaye kuwa Jiji kama ilivyokuwa kwenye Gazeti la Serikali la tarehe 15 Julai, 2016?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, narejea kwenye jibu langu la msingi, kwamba Halmashauri ya Moshi, inahitaji kuleta mapendekezo kwa mujibu wa taratibu zilizoelekezwa na sheria na sisi ofisi ya Rais TAMISEMI, tutafanya tathmini na baadaye kuwasilisha kwa mamlaka husika kwa ajili ya maamuzi husika.
MHE. DAUD P. VENANT: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri yametia moyo kwa wana Igalula. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza, tulishafanya mchakato mara kwanza tukapitia mchakato wote kama alivyoutaja, tulivyofika kwenye hatua ya mwisho kwenye kikao cha RCC, walisema mchakato huo bado. Lakini sasa unavyosema tumepita kwenye mchakato huo huo na tayari document zimetayarishwa kwa ajili ya vikao hivyo, sasa Serikali kupitia kwako Waziri hauoni haja ya kutoa maelekezo kwenye RCC wao sio hatua ya mwisho kutoa maamuzi waziachie document zije Wizara ili ziendelee na machakato mwingine?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Halmashauri ya Wilaya ya Uyui, ni kubwa sana na jiografia yake ni kila unapokwenda unaikuta Uyui. Sasa hamuoni kama Serikali kutoa maelekezo ya kina kwa zile halmashauri ambazo ni zenye competition ili kuweza kuzigawa ili kurahisisha huduma bora kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daud Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema katika swali lake, kwamba walifanya mchakato wa awali, lakini kwa namna moja ama nyingine haukukidhi vigezo lakini wamefanya mchakato wa pili ambao uko ngazi ya mkoa, kwa maana ya kufanya RCC. Sasa tunaelekeza, Mkoa wa Tabora kutekeleza wajibu wao kutimiza sheria hii, kwa maana ya kufanya vikao vya RCC, ili kupitia maombi hayo na baadaye kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kwa kadri ya mwongozo.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kuhusiana na maelekezo ya kugawa halmashauri hii kwa sababu ni kubwa itakuja kulingana na tathmini ambayo itafanyika baada ya RCC kuwasilisha maombi hayo ofisi ya Rais TAMISEMI. Ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Mimi ningependa kujua; kwa vile mchakato wa kupandisha hadhi ya Mji Mdogo wa Mbalizi, ambao ni mamlaka kuwa halmashauri ya mji ilishapitishwa kiwilaya na mchakato vilevile ulishapitishwa kimkoa. Je, ni lini sasa Serikali itaipandisha hadhi hii Mamlaka ya Mji kuwa Halmashauri ya Mji wa Mbalizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante saa. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijiji kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge amesema katika swali lake taratibu za awali za Mbalizi kupandishwa hadhi kuwa Halmashauri ya Mji zilishafanyika, naomba tulichukue hilo tufuatilie kama lilishawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI, na baada ya hapo tutafanya tathmini kwa mujibu wa sheria na tutawapa mrejesho hatua ambayo itafuata. Ahsante.
MHE. OMAR M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi, ina vijiji 102, vitongoji 611, kata 21 na tarafa nne.

Je, ni lini Serikali italigawa Jimbo hili la Kilindi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge twende tukajiridhishe na takwimu ambazo amezisema, tuone vigezo na baadaye tuweze kufanya maamuzi, baada ya tathmini hizo tutawapa mrejesho nini hatua inaweza kufuata baada ya tathmini hiyo, ahsante.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Kwa bahati mbaye, Manispaa ya Mpanda ni kati ya Manispaa zilizopo pembezoni, mwaka jana tulipata walimu sita na watumishi wa afya saba. Serikali inasema nini katika kuinusuru Halmashauri hii na upungufu wa watumishi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, wamekuwepo watu ambao wamekuwa wakijitolea kwa muda mrefu bila kuathiri taratibu za ajira, Serikali inasema nini katika kuajiri watu hawa ambao wamekuwa wakijitolea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Kapufi kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa kuwasemea Wananchi wa Mpanda Mjini na nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutaendelea kushirikiana kwa karibu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimhakikishie kwamba tunajua mwaka uliopita walipata watumishi hawa sita wa elimu na saba wa afya lakini ukiangalia asilimia ya watumishi kwa Mpanda ni asilimia 69.1 angalia kidogo ukilinganisha na Halmashauri nyingine. Lakini hii haimaanishi kwamba hatutaleta watumishi na ndio maana kwenye ajira hizi za mwaka huu bado Mpanda itapata kipaumbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kwa watumishi wanaojitolea Serikali imeweka utaratibu wa kuwapa kipaumbele watumishi wale ambao wanajitolea kwenye vituo vyetu na shule zetu ili ajira zinapotokea waweze kupata ajira kuwa kipaumbele zaidi, ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mhesimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kuniona, naomba niulize swali la nyongeza, je, ni lini Serikali itaongeza watumishi wa afya katika Wilaya ya Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu kwamba Halmashauri ya Meatu ina upungufu wa watumishi na itapewa kipaumbele kwenye ajira hizi ambazo zimekwishatangazwa.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe ina upungufu wa watumishi kada ya ualimu zaidi ya 1,700 ambayo ni karibu asilimia 40 na watumishi karibu 170 ambao ni karibu asilimia 56 kwenye kada ya afya. Je, Serikali iko tayari sasa kwenye ajira zinazokuja hivi karibuni kutoa kipaumbele kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Jimbo la Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya tathimini kuona maeneo yenye upungufu mkubwa zaidi wa watumishi wa elimu, afya na watumishi wa kada nyingine ikiwemo Ukerewe na maeneo haya ndiyo yatakayopewa kipaumbele cha juu zaidi kuliko yale maeneo ambayo yana watumishi wa kutosha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tutatoa kipaumbele Ukerewe, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Waziri ajira mlizotangaza, hakuna option inaonesha wale waliojitolea muda mrefu, mnaweza mkawatambua na kuweza kuwasaidia katika kuwachagua. Ni nini Serikali mtafanya kuhakikisha hao wanaojitolea wanapewa kipaumbele cha kwanza na wengine wanafuata? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaweka utaratibu wa kutoa matangazo kwa ajili ya ajira za watumishi, lakini naomba Mheshimiwa Naibu Spika, Bunge lako tukufu lifahamu kwamba pamoja na watumishi ambao wanajitolea, si watumishi wote waliomaliza vyuo wanaomba kujitolea wanapata nafasi ya kujitolea. Kwa hiyo, bado kuna changamoto ya wale wanaokubaliwa kupata nafasi ya kujitolea. Kwa hiyo, tukiweka kujitolea ya kwamba ni absolute criteria maana yake kuna wale ambao walikuwa na nia ya kujitolea, lakini walioomba hawakupata, watakosa nafasi ya kuajiriwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, na ndiyo tunakwenda kwa utaratibu kwamba tunawapa kipaumbele kwa sababu wanajitolea na Wakurugenzi sasa wanatupa orodha ya watumishi waliokuwa wanajitolea kupitia Halmashauri zetu, lakini na sisi hata ambao hawajajitolea tunawapa criteria ya priority kwa sababu wako walioomba na hawakufanikiwa kupata nafasi hiyo, ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali naomba kuuliza swali la nyongeza. Hospitali ya Wilaya ya Mbinga Halmashauri ya Mbinga Mji ilijengwa mwaka 1970, na mpaka sasa hivi majengo yake yamechakaa. Sasa hivi Serikali ina mpango mkakati wa kuhakikisha hospitali hizo zilizochakaa majengo zinajengwa upya.

Je, lini Serikali itatenga fedha kuhakikisha kwamba majengo mapya yanajengwa katika hospitali ya Mji wa Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunda Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Serikali ya mwaka ujao wa fedha 2022/23 jumla ya shilingi bilioni 16 zimetengwa kwa ajili ya ukarabati au ujenzi wa Hospitali za Halmashauri kongwe na chakavu, ambapo mpango ni kujenga hospitali 19. Kwa hivyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaangalia kama hospitali hiyo ipo kwenye orodha hiyo lakini kama haipo kwenye orodha hiyo tutafanya tathmini ili tuweze kuweka mpango wa kuikarabati hospitali hiyo. Ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Hospitali ya Wilaya ya Ilemela imejengwa lakini mpaka leo hatuna vifaa tiba.

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Ilemela?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha Matondo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba hospitali zetu zote za halmashauri mpya ambazo zimekamilika ujenzi wake zinanunuliwa vifaa tiba ili zianze kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyokusudiwa. Na katika bajetii ya mwaka huu ambao tunamaliza Juni 30, Serikali ilitenga shilingi bilioni 33.5, na fedha zote Mheshimiwa Rais amezipeleka Bohari Kuu ya Madawa (MSD) na tayari taratibu za manunuzi zinaendelea kwa ajili ya vifaa tiba.

Mheshimiwa Spika, pia katika mwaka ujao wa fedha, fedha zimetengwa bilioni 69.95 kwa ajili ya vifaa tiba. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba Hospitali ya Wilaya ya Ilemela ni kipaumbele.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ahsante. Hospitali ya Wilaya ya Tunduru majengo yake ni machakavu kweli kweli; na mingoni mwa hospitali kongwe ile naweza kusema ni namba moja.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutujengea hospitali mpya kama sio kukarabati hospitali ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Tunduru kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ameendelea kuwasemea kwa dhati kabisa wananchi wa Jimbo la Tunduru, na amekuja Ofisi ya Rais - TAMISEMI mara kadhaa kwa ajili ya kuomba ukarabati au ujenzi wa hospitali hii. Na mimi na yeye tumeongea mara kadhaa. Nimhakikishie kwamba kwenye bajeti hii ya 2022/2023 tutaona uwezekano wa kuingiza hospitali hiyo. Na kama tutashindwa kufanya hivyo basi tutafanya kwenye mwaka ujao wa fedha. Ahsante sana.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, asante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Hospitali ya Rufaa Mkoani Rukwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe
Mwakang’ata Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali kupitia Wizara ya Afya ni kuhakikisha mikoa yetu yote inakuwa na hospitali za rufaa za mikoa za kisasa na zenye vifaa tiba. Ninafahamu Hospitali ya Mkoa wa Rukwa ni ya siku nyingi, hivyo, Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirkiana na Wizara ya Afya tutaona mpango wa kuhakikisha inajengwa hospitali au kukarabatiwa ili iweze kuwa na sifa ambazo zinafanana na hospitali ya rufaa ya mkoa. Ahante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Mji wa Bunda imepokea kwa mikono mikubwa uhamasishaji wa Serikali wa ujenzi wa hospitali ili kusogeza huduma ya afya kwa wananchi. Najua wametenga milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya ya halmashauri kwenye Kata ya Bunda Stoo. Je, Serikali kwa mwaka huu wa fedha mko tayari kuwatengea fedha ili wananchi wa Bunda waweze kukamilisha hospitali yao ya mji ambayo iko kwenye Kata ya Bunda Stoo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali inaendelea kujenga hospitali za halmashauri ikiwemo katika Halmashauri ya Mji wa Bunda. Kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema, tayari Serikali imepeleka milioni 500. Mpango huu ni endelevu, nasi tutaendelea kupeleka fedha kwa awamu mpaka majengo yote yakamilike ili wananchi waendelee kupata huduma bora za afya. Ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa suala hili la kugawa Mkoa wa Tabora na kuwa na Mkoa unaitwa Manonga ni la muda mrefu sasa na michakato mingi ilishafanywa ikiwemo jina lenyewe la Manonga. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, Je, hicho kikao cha tarehe 22 kama alivyosema Mheshimiwa Waziri cha RCC kikifanyika, Serikali iko tayari kuugawa Mkoa huu wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imetoa maelekezo na sheria kwamba lazima taratibu hizo zifuatwe na kisha maombi hayo yawasilishwe rasmi Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili iweze kuwasilishwa kwenye mamlaka husika baada ya tathmini. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge baada ya wao kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ofisi itafanya tathmini na kuwasilisha mamlaka husika ili maamuzi yaweze kufanyika kwa kadri itakavyoona inafaa, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mbinga Vijijini, Jimbo la Mbinga Vijijini kutokana na ukubwa wake tulipata ahadi ya Serikali ya kuligawa. Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Benaya Kapinga Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ninawaomba Jimbo la Mbinga kwa maana ya Halmashauri ya Mbinga wapitie hatua zile kwa mujibu wa sheria, wawasilishe hayo maombi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutafanya tathmini lakini tutawapa mrejesho baada ya kufanya tathmini na hatimaye tutawasilisha kwa mamlaka husika, ahsante. (Makofi)
MHE. OMAR M. KIGUA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ambayo yanatia moyo kwa wana Kilindi na Watanzania kwa ujumla. Ninayo maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa Jimbo la Kilindi lina eneo kubwa la utawala; lina vijiji 102, tarafa nne, kata 21 na vitongoji 611, na gari ambalo linatumika sasa hivi ni gari bovu sana. Je, Serikali iko tayari kutuongezea gari lingine baada ya utaratibu huu ambao upo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa utaratibu huu ambao kila Mbunge anaujua hapa kwamba kila halmashauri itapata magari ya wagonjwa kwa mpango wa COVID-19. Je, ni lini utaratibu huo utakamilika ili wananchi wa Tanzania waweze kupata magari hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omar Mohamed Kigua, Mbunge wa Jimbo la Kilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianza kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Omari Kigua kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuwasemea wananchi wa Jimbo la Kilindi. Mimi nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI, tutaendelea kushirikiana naye ili kuhakikisha wananchi wa Kilindi wanapata maendeleo wanayoyatarajia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na ukubwa wa eneo na uhitaji wa gari jingine, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, katika magari haya yanayonunuliwa, jumla ya magari yote yanayonunuliwa kwa ajili ya huduma za afya katika halmashauri zetu zote, ni magari 407. Kwa hiyo tuna magari 195 kwa ajili ya wagonjwa lakini tuna magari 212 kwa ajili ya ajili ya huduma za usimamizi, chanjo na mambo mengine yanayohusiana na afya. Kwa hiyo, kila halmashauri itakuwa na magari mawili.

Mheeshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kutakuwa na magari hayo mapya na ni kabla ya Juni mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhusiana na lini magari hayo yanakuja, taratibu za manunuzi zinaendelea na mpango wa Serikali ni kuhakikisha ifikapo tarehe 30 Juni, magari yawe yamepatikana; au kama atachelewa sana basi ni Julai, lazima magari yatakuwa yamefika kwenye halmashauri zetu, ahsante.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi ya swali la nyongeza. Niipongeze sana Serikali kupitia Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa mpango wake huu wa kununua magari ya wagonjwa katika halmashauri zetu zote nchini, hongera Serikali. Nikiamini pia kwamba Hospitali yangu ya Wilaya ya Kinyonga, pale Kilwa Kivinje tutapata gari hili. Lakini tuna changamoto kubwa ya vituo vyetu vya afya ambavyo havina magari haya ikiwemo Kituo cha Afya Nanjilinji. Je, kwa upendelea wa pekee Ofisi ya Rais- TAMISEMI itapeleka gari ya wagonjwa Nanjilinji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Comrade Ally Kassinge Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Ally Kasinge, kwa kweli anapambana sana kuwasemea wananchi wa Jimbo lake la Kilwa, na sisi tunamhakikishia tutaendelea kuhakikisha tunampa ushirikiano ili wananchi wa Kilwa wapate matunda ya Serikali yao ya Awamu ya Sita. Nimhakikishie, kwamba tunafahamu kwamba Kilwa, nayo itapata gari la wagonjwa, itapata gari la usimamizi, lakini kituo cha Nanjili nakifahamu kiko mbali lakini kinahudumia wananchi wengi. Na katika magari 195 tuna halmashauri 184. Kwa hiyo, tutafanya tathmini na kuona uwezekano wa kuongeza gari Kituo cha Afya Nanjilinji. Ahsante.
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi ya kuuliza swali; na hili swali naliuliza kwa mara ya pili, na ninamuuliza Mheshimiwa Waziri huyu huyu aliyesimama hapa. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Same, ina majimbo mawali; na majimbo mawili haya yameketi kwenye asilimia 40 ya Mkoa wa Kilimanjaro. Hospitali ya Wilaya iko Magharibi ambako ni mbali sana na Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wakifariki huku Mashariki wanapelekwa Mkoa wa Tanga kwa sababu kituo cha afya ni kimoja na hakijakamilika na hakuna hata mortuary mpaka sasa hivi na bado hatuna hata gari la wagonjwa. Mheshimiwa Waziri leo nijibu vizuri nielewe hivi mtaliangalia lini Jimbo langu la Same Mashariki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana sana Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kwa uchapa kazi wake ambao umekuwa mfano hapa Bungeni, na wananchi wa Same Mashariki wana mwakilishi bora kabisa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge uliuliza wiki iliyopita swali hili na leo umeuliza na Serikali hii ni Sikivu, tumepokea tutafanya tathmini tutahakikisha kituo cha afya hicho kinaletewa gari la wagonjwa ili wananchi wapate huduma bora za afya, ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, Wilaya ya Tanganyika ina tarafa tatu na umbali wa tarafa moja hadi nyingine ni zaidi ya kilomita 130, na jiografia yake ni mbaya. Nilikuwa naomba kuuliza Serikali ni lini itaongeza gari la wagonjwa kwenye tarafa ya Kalema, Kabungu na Mwesi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kakoso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ni wilaya kubwa lakini hizi tarafa ambazo amezitaja na nyingine zinahitaji kupata upendeleo wa makusudi kupata gari la wagonjwa. Niseme kwa ujumla, Waheshimiwa Wabunge wote tutafanya tathmini, tunafahamu jiografia ya halmashauri zetu na majimbo zinatofautiana, tutafanya tathmini kwa maeneo ambayo ni makubwa yanahitaji magari zaidi ya moja. Hivyo, kati ya yale magari yanayoongezeka tutapeleka ikiwemo tathmini ya Tanganyika. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru, labda sasa niseme jambo moja, leo ni mara yangu ya tatu nauliza swali hili hili. Mwaka jana kwenye Bunge la bajeti nilijibiwa hivi hivi. Mwaka huu pia Wizara ya Fedha imenijibu kwamba inashughulikia. Ila nimekuwa disappointed na majibu ya Serikali kwa sababu wanasema Wilaya ya Biharamuo haikufuata utaratibu.

Mheshimiwa Mwennyekiti, nina barua hapa ya tarehe 9 Juni, 2020, copy ninayo na ninaamini kila sehemu ipo. Nina barua hapa ya tarehe 20 Agosti, 2020 copy ninayo na barua ipo. Sasa kinachoshangaza ni kwamba, majibu niliyopewa na Wizara hii hii mwaka jana ni tofauti na majibu ninayopewa leo. Nilikuwa naona kwamba tumeshaenda mbele, lakini majibu nayojibiwa leo wananirudisha nyuma tena. Sasa nina maswali mawili ya nyongeza, naomba Serikali inipe majibu hapa wananchi wa Biharamulo wakiwa wamesubiria hospitali kwa muda mrefu.

Ni lini fedha hii inapelekwa? Yaani lini siyo nyuma wala mbele lini, date, kabla ya mwisho wa bajeti hii?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili tuna pesa milioni 376 kwa ajili ya vifaa tiba ya hospitali hii. Sasa, leo ni mwezi wa tano, mwaka wa fedha unaisha. Kwa hiyo tusiletewe hii fedha mwezi wa sita katikati tukaambiwa inatakiwa itumike kwa haraka. Pamoja na hii nijue fedha ya vifaa tiba inakuja lini, na utaratibu wake ukoje kama kama inachelewa tunairudisha au tunabaki nayo? Majibu mawili tu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inafanya kazi kwa kufuata kumbukumbu ambazo zinaoneshwa katika mafaili yetu lakini katika document mbalimbali za Serikali. Na sisi tumefuatilia Wizara ya Fedha na Mipango; pamoja na kwamba Mheshimiwa Mbunge una hizo barua inawezekana ziliandikwa lakini hatuzioni Wizara ya Fedha na Mipango, na suala lilikuwa sio kuandika barua ilikuwa barua zifikishwe Wizara ya Fedha na Mipango.

Kwa hiyo, kama waliandika kwa ku-back date, ili kuweza kutengeneza mazingira hayo sisi hatujazipata hizo, na tungezipata nikuhakikishie Serikali Sikivu ingezifanyia kazi. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tunachosema hapa ni sahihi na tunaendelea kusema vitu sahihi katika Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na lini fedha hizi zinapelekwa katika mwaka huu wa fedha tayari mmepata milioni 300 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Biharamulo. Mwaka ujao wa fedha mmepata milioni 750 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Kwa hiyo, hapa ni wazi kwamba Serikali inaendelea kupeleka fedha na hospitali inaendelea kujengwa. Hitaji la wananchi ni hospitali na Serikali ina commitment kubwa kuhakikisha hospitali inaendelea kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na milioni 376 za vifaa tiba utaratibu upo wazi tunatepeleka fedha Bohari Kuu ya Madawa (MSD) na itanunua vifaa vile ambavyo imeorodheshwa na halmashauri vitaletwa kwa ajili ya huduma hizo. Nikuhakikishie tu, kwamba MSD inakwenda vizuri sana, vifaa vitakuja huduma zitaendelea pale Biharamulo.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti; iko dhamira ya Serikali ya kujenga hospitali za halmashauri 28 katika bajeti ambayo tunaimaliza sasa. Je, lini hospitali hizi zitapelekewa fedha, ikiwemo hospitali ya Halmashauri ya Itigi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Massare, Mbunge wa Manyoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali zote za halmashauri zote ambazo zimeanza ujenzi na vituo vyote vya afya ambavyo vimeanza ujenzi kwa fedha ya Serikali mpango wa Serikali ni kuendelea kupeleka fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa hopitali hizo. Ndiyo maana kwenye mwaka ujao wa fedha tumetenga zaidi ya shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya ukamilishaji wa hospitali zile 59, ikiwemo hii ambayo Mheshimiwa Massare ameisema. Ahsante.
MHE. NOAH L. SAPUTU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza maswali mawili. Kwa kuwa ujenzi wa hospitalli hii na upanuzi wake ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa muda mrefu sasa na haikuweza kutekelezwa.

Je, nini kauli ya Serikali kwa wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ambao wanategemea hospitali hiyo kwa asilimia kubwa na haijajengwa mpaka sasa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Mheshimiwa Naibu Waziri yupo tayari kutembelea hospitali hiyo ili ajionee hali halisi ya wagonjwa walivyo wengi na upanuzi wa hospitali hiyo haikuweza kufanyika kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeza sana Mheshimiwa Noah Saputu, Mbunge wa Arumeru Magharibi kwa namna ambavyo anawasemea kwa dhati wananchi wa jimbo lake. Nimhakikishie kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI itaendelea kushirikiana naye kuhakikisha wananchi wanapata matunda ya Serikali yao sikivu.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ahadi ya Mheshimiwa Rais, ni kwamba ahadi za viongozi wetu wakuu wa nchi ni maelekezo, na ndiyo nimemuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye mwaka ujao wa fedha 2022/2023 tutatafuta fedha ili tuweze kuanza utekelezaji wa ahadi ya Mheshimiwa Rais katika ukarabati hii ya Arumeru.

Mheshimiwa Spika, pili, nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge, tutakubaliana hili baada ya Bunge twende tukaitembelee hospitali hiyo.
MHE. ALEKSIA A. KAMGUNA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kituo cha afya cha Mtimbila kina x-ray lakini hakina jengo la x-ray wala hakina mhudumu wa x-ray. Je, ni lini Serikali itaenda kujenga hilo jengo na hatimaye kupeleka mhudumu ili watu wapate huduma hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aleksia Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba vituo vyetu vya afya ambavyo havina miundombinu ya majengo yanayostahili kuwepo, ikiwemo majengo ya x-ray ni kipaumbele cha Serikali kujenga majengo yale. Kwa hiyo, tutahakikisha kwa sababu tayari kuna x-ray machine katika kituo hiki lakini hatuna jengo, tutaweka kipaumbele ili tuanze ujenzi wa jengo hilo kupitia mapato ya ndani lakini pia tutatafuta fedha Serikali Kuu.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Zahanati ya Kata ya Lumuli ambayo iko katika Jimbo la Kalenga, ziko mbili. Katika Zahanati hizi, wananchi walishapaua na wameshajenga majengo yako vizuri lakini hakuna samani, vitendanishi na vifaa tiba, ni lini Serikali itapelekea hivyo vitu ili wananchi waweze kupata huduma ya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze sana wananchi wa Iringa kwa kujenga zahanati hizi na kuzikamilisha. sasa niseme, kwamba vifaa tiba vinavyohitajika katika ngazi ya zahanati, gharama yake siyo kubwa sana ni imani yangu kwamba mkurugenzi wa halmashauri husika, wana uwezo wa kutenga kati ya ile asilimia 40 na 60 kununua vifaa tiba hivi. Kwa hiyo, naelekeza halmashauri, wakurugenzi watenge fedha, wanunue vifaa tiba zahanati hizi zisajiliwe ziweze kutoa huduma ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Swali langu, ni lini Serikali itatathimini upya uhitaji wa eneo la zaidi ya eka 35, 30 ili kujenga hospitali za wilaya. Ni sehemu zipi utapata eneo kubwa kiasi hicho, kwanini tusitafute namna ya kujenga hizi hospitali hata kuweka ghorofa moja moja badala ya kutafuta eneo kubwa kiasi hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI katika ujenzi wa hospitali za halmashauri yako ya aina mbili. Kuna maelekezo ambayo yanaendana na halmashauri za vijijini, ambako ardhi ni kubwa wanahitaji kutenga angalau ekari 30 na kuendelea kwa sababu hospitali zile tunazojenga tunatazama miaka 50 au mia moja ijayo, haituangalii miaka mitano au kumi ijayo. Kwa hiyo, tunahitaji kuwekeza katika maeneo makubwa ili hata baada ya miaka 100 miundombinu tu itabadilika lakini eneo litaweza kutosheleza.

Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ya mijini tunaweka eneo siyo kubwa sana, inategemeana na eneo, lakini tunapendekeza kujenga majengo ya kwenda juu kwa maana ya maghorofa. Kwa hiyo, maeneo yote mawili yametazamwa, maeneo ya mijini, tunakwenda kwa maghorofa, kama eneo halitoshi lakini maeneo ya vijijini tunataka angalau eka 30 kwa sababu tunaona miaka mingi ijayo.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina swali la nyongeza.

Katika vikundi hivyo 6317 kwa upande wa Zanzibar ni vingapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, Mbunge wa Jimbo la Bububu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze sana kwa kazi nzuri kubwa anayoifanya, lakini naomba niichukue hili ili tukafanye mchanganuo kuona kwa upande wa Zanzibar vilikuwa vikundi vingapi kati ya hivi vilivyoainishwa.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Wengi wanaochukua mikopo hiyo ni pamoja na kinamama ambao wanakuwa na vikundi vyao vya vikoba, lakini hela zao huwa zinazunguka kwenye makasiki na wakati mwingine kasiki linaibiwa.

Ni lini sasa Serikali itazungumza na mabenki ili waweze kuongezewa angalau asilimia moja ya kuweka kwenye account zao kuendesha viofisi vidogo dogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba akina mama na vikundi vingine na hususani akina mama wanakopa lakini pia wana shughuli za vikoba, na kuna risk hizo za mara nyingine kupoteza fedha kwa njia mbalimbali. Nimepokea wazo lake, tumepokea kama Serikali tutalifanyia tathmini kuona namna ya kuongea na benki ili tuone njia sahihi ambayo inaweza kufanyika kunusuru changamoto.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Spika, ahsane kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuhakikisha vile vikundi vya wanawake na vijana ambao wanapata mikopo ili mikopo hiyo isipotee wafanyiwe tathmini ya kazi wanazokwenda kuzifanya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Agnes Hokororo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kabla ya vikundi hivi vya wanawake, vijana na wenye ulemavu havijapewa mikopo, moja ya kigezo muhimu ni kufanya tathmini ya uwezo lakini na utayari wao wa kuanza kufanya shughuli hizo za ujasiliamali ili kuhakikisha zile fedha wanazokopeshwa zinaleta tija, lakini pia hazipotei. Tumeendelea kufanya hivyo na ndiyo maana tumeona matokeo mazuri ya urejeshaji ukiangalia kwa miaka inavyokwenda mpaka sasa kuna improvement kubwa na tutaendelea kufanya hivyo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa vikundi vingi ambavyo vinapata mkopo wengi wanatoka maeneo ya mijini. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba elimu inatolewa ili wanawake na vijana wa vijijini pembezoni waweze kupata mkopo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika halmashauri zetu zote zikiwemo za vijijini kuna fungu ambalo linatengwa kupitia maafisa maendeleo ya jamii kwa ajili ya kuhamasisha, kuelimisha, wanawake vijana na watu wenye ulemavu kunufaika na fursa za mikopo hiyo. Kwa hiyo suala hilo tunalifanya na jambo kubwa ambalo tunaendelea kulifanya ni kuongeza nguvu ili wananchi wapate nguvu ya kutosha waweze kunufaika na mikopo hiyo.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Spika, ninashukuru sana kwa majibu ya Serikali. Swali langu la msingi liliuliza kada zote hadi sasa kada za watendaji wa kata, vijiji na mitaa hazijapata kibali. Halmashauri ya Mji wa Mbulu ina upungufu wa watendaji wa kata, vijiji na mitaa zaidi ya 70, ni miaka mitatu sasa.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuajiri watumishi hawa katika Halmashauri wa Mji wa Mbulu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa kuwa waalimu wa sayansi katika mgawo wa ajira mbili zilizopita za Serikali hawakupatikana katika Halmashauri wa Mji wa Mbulu kwa kigezo cha kuona waalimu wa sanaa ni wengi na wanafunzi wameendelea kukosa masomo ya sayansi. Je, Serikali ina mkakati gani au inakusudia kugawa walimu wangapi wa sayansi katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kada ambazo hazijatangazwa kwa maana ya watendaji wa kata wa vijiji na mitaa lakini na kada nyingine zote zitaendelea kutangazwa kwa awamu kwa sasa tumeanza na sekta ya afya na elimu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge lengo la Serikali ni kuhakikisha kada hizo nyingine pia zinaajiriwa. Lakini pamoja na hiyo bado halmashauri zimeendelea kuajiri watendaji kupitia mapato ya ndani, baadhi ya halmashauri wataendelea kufanya hivyo kwa vibali vya Serikali Kuu pia kupitia Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na walimu wa sayansi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika ajira hizi ambazo tayari zimetangazwa za walimu 9800 tutaenda kuhakikisha tunapeleka walimu wa sayansi katika maeneo yenye upungufu mkubwa zaidi wa walimu wa sayansi. Kwa tathmini hiyo tumeshaifanya na tutampa kipaumbele katika Jimbo lake la Mbulu Mjini, ahsante.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwa swali hili zuri sana la nyongeza lililoulizwa na Mheshimiwa Mbunge, kwanza naomba kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge, kwa kibali ambacho Mheshimiwa Rais amekitoa cha kuhakikisha tunatoa ajira 32,604 ambazo zilipangwa kwenye bajeti ya mwaka 2021/2022, baada ya kutoa ajira zile za kipaumbele kwenye sekta ya afya, sekta ya elimu na sekta zile nyingine ambatanishi. Mheshimiwa Rais kupitia ofisi yetu ameridhia sasa kada zile nyingine za watumishi zilizobakia ikiwemo hao watendaji wa vijiji na kata ziweze kufanyiwa mgao kwenye ajira 7,792 ambapo bado hizo zinasimamiwa na Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba waajiri wote nchini wahakikishe tu wanapanga majukumu sahihi kwa watumishi wote wapya watakaoajiriwa ili waweze kuongeza tija na kutekeleza majukumu yao ipasavyo. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Jimbo la Mbulu Vijijini lina uhaba mkubwa wa Afisa Maendeleo ya Jamii pamoja na Walimu wa Sayansi: -

Je, katika mgao huu ukoje? Mtaangalia majimbo haya ya vijijini ili kuweka mgao sawa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba katika ajira ambazo hivi sasa zinaendelea na utaratibu wa kuajiri, tumeshaainisha maeneo yenye upungufu mkubwa wa wataalamu; wataalamu wa maendeleo ya jamii na pia wataalamu kwa maana ya Walimu wa Sayansi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kufuatia tathmini ile, tutahakikisha tunatoa kipaumbele katika maeneo yenye upungufu mkubwa zaidi ikiwemo katika Jimbo la Mbulu Vijijini. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Ni kwanini sasa Serikali haina mikakati ya kuhakikisha kwamba halmashauri zenye vyanzo vidogo vya mapato iweze kuwa inawapa fedha nyingi kuliko ambazo zinatengwa ukilinganisha na halmashauri nyingine?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kwanini Serikali isitumie vigezo vya ukubwa wa eneo ili kuhakikisha kwamba inatoa fedha kulingana na kipaumbele, kulingana na ukubwa wa eneo husika, kuliko wanavyofanya sasa hivi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na vyanzo ambavyo halmashauri wanakusanya kwa mapato ya ndani vinatofautiana kati ya halmashauri moja na nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hoja ya Mheshimiwa Mbunge, kwamba zile halmashauri zinazopata mapato kidogo ya ndani zipewe fedha zaidi. Ni kwamba suala hili linakwenda kuzingatia pia mara nyingi, ukiziona halmashauri hizi zenye mapato madogo ni halmashauri pia ambazo zina population ndogo lakini pia zina shughuli za kibiashara ndogo zaidi ukilinganisha na halmashauri zenye mapato makubwa kwa sababu mapato yanatokana na shughuli za kiuchumi katika halmashauri husika.

Kwa hiyo, utaratibu wa kupeleka fedha unazingatia pia population ya eneo husika, lakini pia na shughuli zile, kwa mfano miradi ya kimkakati ambayo ilitakiwa kwenye kuwekezwa kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tutaendelea kufanya tathmini kuona uwezekano wa kuongeza zaidi package za maendeleo kwa halmashauri zenye mapato madogo, ukilinganisha na halmashauri zenye mapato makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na kuzingatia ukubwa wa eneo la kijiografia, suala hili linategemeana na ukubwa lakini pia population kwa sababu fedha za maendeleo zinapelekwa kwa ajili ya kusaidia wananchi. Kuna halmashauri ambazo ni kubwa sana zina maeneo ya hifadhi za misitu na kadhali. Kwa hiyo, ukiangalia tu ukubwa wa jiografia utapeleka fedha nyingi eneo ambalo lina population ndogo kwa sababu tu kuna ukubwa wa jiografia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunazingatia yote, ukubwa, population lakini pia na shughuli zingine za kimaendeleo.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Serikali imekuwa ikitoa fedha za maendeleo kwenye halmashauri wakati mwingine imekuwa ikitoa fedha mwezi ambao unakaribia mwisho wa mwaka wa fedha kuisha.

Je, Serikali imetatua vipi changamoto hii ya kuchelewesha fedha kwenye halmashauri na baadaye kuzirudisha hazina?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE.DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha ambazo zinapelekwa kwenye halmashauri zetu karibu na mwisho wa mwaka wa fedha mara nyingi zimekuwa zikirejeshwa kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maelekezo mahususi yametolewa, kuhakikisha kwamba halmashauri ambazo zinapokea fedha karibu na mwisho wa mwaka wa fedha, ziandike barua kupitia ofisi ya Rais TAMISEMI, kwenda Wizara ya Fedha na Mipango, siku 15 kabla ya tarehe 30 ya mwaka husika, ili zile fedha zisirejeshwe ziendelee na miradi, kwa maana ya quarter ya kwanza ya mwaka wa fedha unaofuata.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana na nishukuru kwa majibu ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kituo hiki cha Mapela, ndio kituo pekee cha Serikali katika Halmashauri ya Mbinga Vijiji ambayo ina kata 29. Hicho kituo cha Maguo alichokitaja Mheshimiwa Naibu Waziri ni kituo cha Mission, tu nashukuru wanatusaidia, sina hakika kama gharama zake zinalingana, sina hakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti nina maswali maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini Serikali itapeleka wahuduma wa afya, katika zahanati saba Kipolopolo, Lukiti, Kihuruku, matuta, Mwihayo, Ikwela na Lituru; zahanati hizi nimeuliza mwaka jana swali hapa. Lini zitafunguliwa maana wananchi wamejenga na wamekamilisha, lini sasa zitafunguliwa ili ziweze kutoa huduma kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Halmasauri ya Mbinga, ina upungufu mkubwa wa watumishi, zaidi ya asilimia 80 hatuna watumishi. Je, katika mgao huu unaokuja, Serikali ipo tayari kuwaonea huruma na kutoa kipaombele katika halmashauri ya Wilaya ya Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Mbinga Vijijini ina kata 29 na ina kituo kimoja cha afya; lakini nimuhakikishie Mheshimiwa Rais wetu mama Samia Hassan ameweka mkakati wa uhakika wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati katika kata za mkakati na tarafa za kimkakati. Tulishakuomba na ulishaleta hapa orodha ya kata ambazo zitajengewa vituo vya afya. Nikuhakikishie Serikali hii sikivu tutahakikisha tunajenga vituo vya afya katika Jimbo la Mbinga Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kuhusiana na watumishi kuhitajika katika zahanai saba; kwanza niwapongeze sana wananchi wa Mbinga Vijijini kwa kutoa nguvu kujenga zahati saba ambazo zimekamilika, lakini na Serikali ilichangia. Nimhakikishie kwamba tunakwenda kuzisajili zahanati hizi. Kwa upande wa ajira hizi ambazo zimetangazwa tutakwenda kutoa kipaumbele kikubwa kwenye halmashauri zote zenye upungufu mkubwa wa watumishi ikiwepo Halmashauri ya Mbinga Vijijini. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI E. KINGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa fedha hizi asilimia kumi zinazotolewa kama mikopo zinatokana na tozo pamoja na kodi ambazo wananchi kwa ujumla wengi wanashiriki kuzitoa na zinazokusanywa katika halmashauri yetu;

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuwapitia vijana wote mikopo bila kuwabagua, kama vile Serikali vijana wengi waliojiajiri katika sekta za uzalishaji, ujasiriamali, kilimo na boda boda,?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa wanaume, kwa maana ya akina baba nao pia wamekuwa wakijishughulisha na shughuli za uzalishaji. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kuwapatia nao mikopo bila kuwabagua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Elibariki Kingu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba asilimia kumi inatokana na mapato ya ndani na inagusa makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Na niseme dhahiri kwamba mikopo hii haina ubaguzi wowote kwa vijana, kwa wanawake, wala watu wenye ulemavu. Suala ambalo wanatakiwa kufanya kwa mujibu wa sheria na kanuni za asilimia kumi ni kuomba kupitia vikundi vyao vya ujasiriamali. Na vijana wote wanaomba kupitia vikundi na wakawa na sifa hizo hakuna anayebaguliwa, wote wanapewa mikopo hiyo katika mazingira ya halmashauri zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tutaendelea kuhakikisha kwamba tunawapa fursa vijana wote wanawake na watu wenye ulemavu ili waweze kujiendeleza katika shughuli za kiujasiriamali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na suala la wanaume, utoaji wa mikopo hii ni kwa mujibu wa sheria, na sheria yetu ambayo tuliipitisha katika Bunge hili ilisema vijana, wanawake, na watu wenye ulemavu. Vijana ni umri wa chini wa miaka 35, lakini hoja ya msingi ni kwamba wanaume walio wengi ukilinganisha na makundi haya tayari wanauwezo wa kuwa dhamana, kwa maana ya ardhi, majengo na biashara ambazo zinaweza kutumika kama collateral kwenye mikopo ukilinganisha na makundi haya. Ndiyo maana tuliweka kipaumbele kwa wanawake, vijana, na watu wenye ulemavu kwa sababu hawana collaterals zinazowawezesha kupata mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kufanya tathmini kuona uwezekano wa kuingiza wanaume kwa kadri itakavyoona inafaa. Ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa walemavu hawa si wote wana uwezo wa kufanya shughuli za kibiashara ama kujiwezesha kiuchumi lakini wanalelewa na babu zao, bibi zao ama baba zao ama wajomba zao ambao hawa-qualify katika hii asilimia kumi.

Je, Serikali haioni wakati umefika sasa wakuangalia wazazi ama walezi wanaoangalia walemavu ambao wenyewe hawajiwezi lakini wanaweza kuwezeshwa kwa ajili ya kuangalia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna walemavu ambao hawana uwezo wa kufanya shughuli hizo na wangehitaji kupata mikopo ili wajikwamue kiuchumi. Naomba tuchukue wazo la Mheshimiwa Mbunge, tukalifanyie tathmini na kuona uwezekano wa kuwapa mikopo hiyo wazazi au walezi wa hao wenye ulemavu ili waweze kuwasaidia. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kutokana na majibu ya msingi ya swali hilo, Mheshimiwa Waziri ameendelea kusisisitiza kwamba mikopo hiyo inatolewa kwa vikundi; na kwa kuwa hiyo dhana ya vikundi imekuwa ni mwiba sana kwa wale akina mama wa Kilimanjaro wanaotaka kuchukua mikopo hususan wale ambao wako katika ujasiriamali.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kurekebisha kipengele hicho ili mikopo hiyo itolewe kwa mtu mmoja mmoja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakwenda kuipitia sheria na kanuni ya mikopo ya asilimia kumi. Katika kupitia kanuni hii tayari tumeshaanza kufanya tathmini kwa kina ili kuona maeneo gani yanahitaji kuboreshwa zaidi likiwemo suala la kuona uwezekano wa mtu mmoja kupata mkopo badala ya vikundi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, baada ya tathmini hiyo, tutafanya maamuzi na kuona utaratibu sasa utakuwa wa aina gani. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba nifanye masahihisho kidogo, kituo kinaitwa

Rukalagata, Kata ya Biharamulo Mjini, kingine ni Kalenge Kata ya Kalenge na kingine ni Nyabusozi Kata ya Nyabusozi.

Mheshimiwa Spika, tarehe 9 Novemba 2022 nilisimama hapa ndani nikiongelea Kituo cha Rukalagata kwamba hakina jengo la upasuaji na bahati nzuri nikajibiwa na Waziri wa Fedha kwamba nilete maombi maalum na wao watanitengea pesa kwa sababu hospitali ya Biharamulo Mjini imejengwa lakini iko nje ya Mji kwa hiyo watu wa Biharamulo Mjini hawapati huduma. Barua yetu ilitoka Tarehe 14 siku tatu zilizofuata…

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa Ezra ni lipi?

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Swali la kwanza je, hii barua ilishapokelewa na imefika kwa Waziri wa Fedha? Je, status ikoje, kama haijafika naomba niikabidhi hii barua.

Pili, napenda nishukuru kwa sababu nimeambiwa vituo viwili vitafanyiwa kazi. Ni hayo tu. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimepokea marekebisho, pili kwa kuwa barua iliwasilishwa na Halmashauri ya Biharamulo kwenda Wizara ya Fedha, Ofisi ya Rais -TAMISEMI tutafanya mawasiliano ya karibu na Wizara ya Fedha baada ya maswali hapa na tuone kama barua imeshafika na tuone hatua za utekelezaji ili ahadi ya Serikali ya kuleta fedha hiyo iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, pili, hivi vituo vya afya viwili ambavyo vimetengewa shilingi milioni 500 ni vile kati ya vituo vya afya vitatu ambavyo Halmashauri mtaona kipaumbele ni vipi vianze ili tuanze kukarabati na kuanza kutoa huduma hizo. Ahsante. (Makofi)
MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nami naomba niulize swali la nyongeza.

Je, katika hizo fedha shilingi bilioni 8.75 Kituo cha Afya cha Nkhomola kitakuwa ni miongoni mwa vituo vya kupatiwa hizo pesa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rose, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ambazo zimetengwa shilingi 8,750,000,000 zitakwenda kuainisha vituo vya afya 20 vyenye uchakavu wa hali ya juu zaidi. Kwa sababu sina orodha hapa naomba kwa ridhaa yako baada ya kipindi hiki nitaangalia na kuona kama kituo hicho ambacho amekitaja Mheshimiwa kipo kwenye orodha hiyo, ahsante.
MHE. JULIANA D SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru; wananchi wa Kata ya Sanga katika Wilaya ya Mbozi wamejenga boma la kituo cha afya; je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa kituo hicho? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata ya Sanga ambayo wananchi wamejenga boma kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya ni sehemu ya Kata nyingi kote nchini ambazo wananchi wamejenga, Serikali imeweka mpango mkakati, kwanza kukamilisha vituo vya afya ambavyo ujenzi wake umeanza lakini baada ya kukamilisha vituo hivyo tutakwenda awamu ya pili ya kuainisha maboma na kuanza kuyakamilisha na wakati huo tunatoa kipaumbele pia katika jengo hili la kituo cha afya cha Sanga, ahsante. (Makofi)
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi; kwanza ninaipongeza Serikali imejenga vituo vya afya vingi sana ndani ya Halmashauri ya Tanganyika, tuna tatizo la ukosefu wa vitendea kazi kwenye vituo vya afya pamoja na watumishi.

Je, ni lini Serikali itapeleka vitendea kazi na watumishi kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini, Kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba vituo vingi vya afya vimejengwa lakini katika mwaka wa fedha huu Serikali imetenga zaidi ya bilioni 193 kwa ajili ya kupeleka vifaatiba katika vituo vilivyojengwa. Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwamba kwa kiasi kikubwa vituo vyetu vimeanza kupokea fedha na vifaatiba kwa ajili ya kutoa huduma.

Mheshimiwa Spika, ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hili litaendelea katika vituo vya afya vya Halmashauri ya Tanganyika. Ahsante sana.
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; Zahanati ya Mongo la Ndege imejengwa kwa kipindi kirefu tokea nikiwa Diwani wa Ukonga.

Je, Serikali haioni sasa kutokana na ongezeko la wakazi kwenye mtaa wa Mongo la Ndege na maeneo jirani ya Jimbo la Segerea ni wakati sasa wa kupandishwa hadhi na kuwa kituo cha afya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Jimbo la Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Zahanati ya Mongo la Ndege inahitaji kupanuliwa na kupandishwa hadhi kuwa kituo cha afya, kwa awamu hii tunaendelea kwanza na ukamilishaji wa zahanati na vituo vya afya ambavyo kazi ya ujenzi imeanza.

Mheshimiwa Spika, ninatoa wito kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala kuona uwezekano wa kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza kupandisha hadhi kituo hiki cha afya cha Mongo la Ndege. Ahsante. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata ya Uyui ambayo ndiyo kata kubwa kuliko kata zote katika Jimbo la Tabora Mjini haina kabisa kituo cha afya na tulikwishaomba muda mrefu ili iweze kupata kituo cha afya.

Je, ni lini Serikali itatupatia kituo cha afya katika Kata hiyo ya Uyui?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kata zote ambazo zina vigezo vya kujengewa vituo vya afya zitaingia kwa awamu baada ya kukamilisha vituo vya afya ambavyo vinaendelea kujengwa. Serikali imekwishatoa maelekezo kwa Halmashauri zenye mapato ya ndani yanayozidi bilioni tano, kuanza ujenzi wa vituo hivyo kwa kutumia ile asilimia 60 na asilimia 70 ya mapato ya ndani. Kwa hiyo, nitoe maelekezo pia kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora kuanza kutenga fedha kwa awamu, wakati Serikali pia inatafuta fedha kwa ajili ya kupandisha hadhi lakini pia kujenga kituo cha afya katika kata hii, ahsante.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Kata ya Makanya katika Jimbo la Same Magharibi kimechakaa sana na ni cha zamani sana.

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha katika Halmashauri ya Wilaya ya Same ili kukarabati kituo cha afya cha Makanya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Mathayo Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Makanya ambacho amekitaja Mheshimiwa Mbunge ni sehemu ya vituo ambavyo ni chakavu na Serikali inaendelea kuweka mpango mkakati wa kuvikarabati. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aamini kwamba Serikali imetambua hilo, tunaweka mpango endelevu wa kukarabati na kituo hiki kitapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bweri ni kati ya vituo vya afya vya kwanza cha kwanza kujengwa pale katika Manispaa ya Musoma lakini hakikukamilika na kimechakaa sana pamoja na kituo cha Makoko.

Je, ni lini sasa Serikali itatoa fedha ili tuweze kuvimalizia vituo hivyo viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya ambavyo Mheshimiwa Mbunge amaevitaja, kituo cha Bweri na Makoko ni sehemu ya vituo ambavyo Serikali inaweka utaratibu mahsusi kwa ajili ya kutenga fedha na kuvikarabati, vile ambavyo miundombinu haijakamilika vinatengewa fedha kwa ajili ya ukarabati na kujenga majengo hayo. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa kuwa mikopo hiyo kutokuwa na riba ni kivutio kikubwa sana kwa wale ambao hawana uwezo; na wakati huo huo wanawake wana vikoba: Je, Serikali inaonaje sasa kama wale wa vikoba watapatiwa mikopo hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shally Raymond Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sheria ya mikopo ya asilimia kumi imeeleza kwamba wajasiriamali wanawake, vijana na watu wenye ulemavu wanaweza kukopeshwa wakijiunga kwenye vikundi vyao na mkopo huo hauna riba. Kwa hiyo, kama wanawake walio kwenye vikoba ni sehemu ya kikundi cha wajasiriamali bila kujali kwamba wapo kwenye vikoba au la, wataweza kukopeshwa fedha hizo kwa utaratibu huo na kufanya shughuli zao ili kujiletea maendeleo, ahsante. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, asilimia 10 tuliipitisha kwa mabadiliko ya Sheria ya mwaka 2019, lakini Taarifa za Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kuhusiana na asilimia 10 ya mwaka 2021 zilipotea shilingi bilioni 47.5; za mwaka 2021/2022 iliyotoka juzi, zimepotea shilingi bilioni 88.

Mheshimiwa Spika, swali langu kwa Waziri; kwa kuwa Wakurugenzi ambao ndio accounting officers wamepewa majukumu ya kusimamia hizi fedha kuhakikisha zinawafikia watu sahihi, lakini Wakurugenzi hawafanyi hivyo, matokeo yake fedha nyingi zinapotea: Ni lini Serikali inapanga kuchukua hatua kali za kisheria dhidi ya accounting officers huko kwenye Halmashauri zetu wanaoshindwa kutekeleza majukumu yao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli moja ya changamoto kubwa katika mikopo ya asilimia 10 ni kasi ya maejesho kwa vikundi vilivyokopeshwa. Serikali imetambua changamoto na ndiyo maana katika miaka mitatu mfululizo, kasi ya urejeshaji imetoka asilimia 62 mwaka 2018/2019 mpaka asilimia karibu 80 mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Spika, pamoja na changamoto hiyo Serikali imeendelea kuchukua hatua kwa accounting officers, kwa maana ya Wakurugenzi katika Halmashauri zetu ambao walithibitika kutosimamia ipasavyo marejesho ya mikopo ya asilimia kumi. Zoezi la kuchukua hatua kwa accounting officers ni endelevu. Kila mara Serikali itakapotambua kwamba kuna Mkurugenzi hajatimiza wajibu wake na fedha hazijarejeshwa, lazima atachukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu za utumishi na kwa mujibu wa taratibu za kisheria, ahsante.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nataka kujua kwa kuwa kasi ya utoaji wa fedha hailingani na uhitaji wa maboma yanayohitajika kwa zahanati kwa vijiji vyote. Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu kwa mwaka huu wa bajeti kutenga fedha kukamilisha maboma yote ambayo yanahitajika kwenye vijiji vilivyohitaji ujenzi wa zahanati?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Serikali imekuwa ikitenga fedha shilingi milioni 500 mpaka shilingi milioni 700 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwenye kata 26 kwenye jimbo moja. Je, Serikali haioni sasa badala ya kupeleka fedha hizi kwenye umaliziaji wa kituo cha afya kimoja, fedha hii iende kukamilisha maboma yote yaliyojengwa na nguvu za wananchi kwenye eneo hilo hilo la jimbo ambao wanaweza wakakamilisha maboma 14 badala ya kituo cha afya kimoja kwenye eneo moja la wilaya moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Jimbo la Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kasi ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati nchini kote kwa kweli ni kubwa na Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameweka kipaumbele cha hali ya juu sana katika sekta ya afya na ndiyo maana katika kipindi cha miaka hii miwili zaidi ya maboma 1,600 ya zahanati yamekamilishwa na zahanati hizo zimeanza kutoa huduma. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kasi hii ya Serikali itaendelea ili kuhakikisha kwamba maboma hayo ambayo bado hayajakamilishwa yanakamilishwa na kuanza kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na kuacha kujenga vituo vya afya na kuweka kipaumbele kwenye zahanati, mfumo wa huduma za afya una utaratibu wa rufaa kwa ngazi. Ngazi za zahanati zina umuhimu wake katika ngazi ya vijiji lakini ngazi ya vituo vya afya ni rufaa ya zahanati na tunafahamu zahanati hazifanyi upasuaji na hazilazi kwa hiyo lazima tuendelee na nguvu za kujenga vituo vya afya sambamba na ujenzi wa zahanati.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nilitaka kujua ni vigezo vipi vinatumika katika kugawa hizo fedha za umaliziaji wa maboma ya zahanati kwani Jimbo la Mbozi tuna maboma zaidi ya 20 lakini kiasi kinachokuja ni kidogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vigezo ambavyo vinatumika kupeleka fedha ni idadi ya watu, umbali wa kijiji hicho kwenda kwenye kijiji chenye zahanati cha jirani zaidi. Lakini katika Jimbo la Mbozi pia Serikali imeendelea kupeleka fedha na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kupeleka fedha pia.
MHE. GEORGE N. RUHORO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Ngara bado lina kata nyingi hazina vituo vya afya, je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha tunapata vituo vya afya kwenye kata hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA- (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ndaisaba George, Mbunge wa Jimbo la Ngara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshafanya tathmini na kuainisha maeneo ya kimkakati ya kujenga vituo vya afya ikiwemo katika Kata za Jimbo la Ngara.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, boma la zahanati ya Isusumya limekuwa la muda mrefu sana na tulileta maombi maalum. Nataka kujua sasa mpaka leo hatujajua nini kinaendelea, nini mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba zahanati hiyo imekamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimuelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri ya Chemba kutenga fedha za ukamilishaji wa Boma shilingi milioni 50 kwenye mwaka wa fedha ujao ili kukamilisha boma hili ambalo halmashauri imeona ni kipaumbele na tayari imeshaleta maombi maalum kwa ajili ya ukamilishaji.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Serikali imekuwa ikitoa kiwango cha fedha kinachofanana katika umaliziaji wa maboma yote bila kuangalia hali halisi ya gharama za ujenzi.

Je, hamuoni kuna haja ya kufanya tathmini ili kutoa fedha kulingana na gharama ya ujenzi na maeneo husika ili maboma yaweze kukamilika kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa tukitoa fedha kwa kiwango kinachofanana kwa maeneo tofauti na hivi sasa Serikali inafanya tathmini ya kutoa bei au BOQ kulingana na maeneo kijiografia, umbali lakini pia na gharama kutokana na maeneo hayo.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Kituo cha Afya cha Kata ya Ukumbi pamoja na Zahanati ya Kijiji cha Ilutila ni miaka 16 sasa ni maboma. Je, ni lini Serikali itamalizia kituo hicho cha afya pamoja na hiyo zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Justin Nyamoga, Mbunge wa Jimbo la Kilolo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilishaweka utaratibu na tulishawaelekeza Wakurugenzi wa halmashauri kuleta vipaumbele vya maboma hasa ya vituo vya afya lakini pia na zahanati ambazo zinauhitaji mkubwa katika maeneo hayo. Kwa hiyo, nimwelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilolo kuwasilisha rasmi Ofisi ya Rais, TAMISEMI maombi ya vituo hivi ili Serikali iweze kuona namna ambavyo Serikali itatafuta fedha lakini pia na mapato ya ndani yatachangia kukamilisha vituo hivyo.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kijiji cha Ndihuli kilichopo Kata ya Magulilwa kilijenga boma zaidi ya miaka saba. Je, ni lini sasa Serikali itatuonea huruma ipeleke fedha hapo tuweze kumalizia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge awasilishe maombi hayo kupitia kwa Mkurugenzi ili tuweze kuona namna ambavyo tutatenga fedha kwenye bajeti za miaka ijayo kwa ajili ya kukamilisha boma hili kwa ajili ya zahanati.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante, Jimbo la Tunduru Kusini lina maboma saba yako katika hatua mbalimbali katika Vijiji vya Mkapunda, Chuwala, Ukandu, Nazya pamoja na Lupanji; je, Serikali ina mpango gani sasa wa kupeleka fedha kumalizia maboma hayo ya zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Mpakate, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumekwisha elekeza na nirudie kuwakumbusha Wakurugenzi wa halmashauri kuhakikisha wanaweka vipaumbele vya ujenzi na ukamilishaji wa maboma ya zahanati katika maeneo yenye uhitaji mkubwa. Kwa hiyo, maboma haya saba ambayo Mheshimiwa Mbunge ameyataja, Ofisi ya Rais TAMISEMI tutachukua lakini tutafanya mawasiliano na Wakurugenzi ili tuone yapi tuanze nayo kwa awamu lakini tutaendelea kutenga fedha kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kuna boma la Mji mwema, Mkalanga pamoja na Kata ya Kivavi, ni lini Serikali itamalizia maboma ambayo wananchi wameshayajenga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, boma hili la Mji mwema lakini na Mkalanga ni maboma ambayo tayari tulishayaingiza kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakwenda kutekeleza ukamilishaji wa maboma hayo mwaka ujao wa fedha.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi. Wananchi wa Kata ya Nyasaka Mtaa wa Kiloleli B wamenunua kiwanja kwa ajili ya kujenga zahanati. Je, ni lini Serikali itawajengea zahanati katika kiwanja hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niwapongeze Kijiji hiki kwa kununua eneo kwa ajili ya ujenzi wa zahanati lakini nimwelekeze Mkurugenzi kuanza kutenga fedha kwa awamu kwa ajili ya ujenzi wa zahanati hii.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa kumekuwa na mkanganyiko wa kutoa huduma za kijamii kwenye eneo ambalo lina utawala wa aina mbili, Ofisi ya Mambo ya Ndani na Ofisi ya TAMISEMI na wanaotoa fedha ni TAMISEMI. Je, mkanganyiko huu ni lini Serikali itakwenda kuuondoa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa Umoja wa Mataifa ulijitoa kuhudumia kambi za wakimbizi na kukabidhi Serikali na Serikali ikatoa uraia. Tunavyozungumza leo hii eneo la utawala kata tayari kuna madiwani ambao wanafanya shughuli za kiutawala lakini eneo la Serikali za vijiji hakuna utawala wa aina yoyote. Ni lini mtakaa na Wizara ya Mambo ya Ndani ili muondoe sintofahamu ambayo ipo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkanganyiko ambao umetokana na vijiji hivi kuwa chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na Ofisi ya Rais TAMISEMI kimsingi tunaendelea kuiweka sawa; na ndiyo maana siku za nyuma hatukuwa na madiwani katika zile kata nne lakini mwaka 2020 madiwani walichaguliwa. Pia kuna watendaji wa vijiji ambao siku za nyuma hawakuwepo; na linaloendelea sasa ni utaratibu tu wa ndani ya Serikali kuongea kati ya Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ili tuweze kukubaliana mfumo mzuri zaidi wa kuendesha vijiji hivyo.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakaa na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kuondoa changamoto ambayo ipo kwa sasa, ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Waziri kwa majibu mazuri ya Serikali; nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali iko tayari kukipa kipaumbele kipande kile cha kilomita nne kutoka barabara kuu ya Nzega kwenda kituoni ili kiweze kufikika wakati wa dharura?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Je, Serikali sasa iko tayari kumalizia kipande cha barabara kinachotokea pale kituo cha afya kwenda Kijiji cha Kasenga, Majengo, Ikongolo, Ipuge; vilevile vijiji vya Izugawima, na Nzuguka ili wananchi wa vijiji vile waweze kupata huduma haraka kwenye Kituo cha Afya cha Upuge?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iko tayari kuipa kipaumbele barabara hiyo ya kilomita nne ili kuweza kusogeza huduma za jamii kwa wananchi. Nimwelekeze Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Uyuwi kuhakikisha kwamba wanatenga fedha kwenye eneo hilo, kwa maana ya kuipa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa kuwa barabara hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja, ambayo inaunganisha kituo cha afya na vijiji kadhaa alivyovitaja ni muhimu kuwawezesha wananchi kupata huduma za afya Serikali iko tayari kuipa kipaumbele barabara hii ili iweze kujengwa na kupitika vizuri. Ahsante.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, je, ni lini barabara ya Ihanda-Ipunga hadi Chinji itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Hasunga, Mbunge wa Jimbo la Vwawa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilishawaelekeza mameneja wa TARURA katika wilaya zetu kuhakikisha wanatenga vipaumbele vya barabara ambazo zinahitaji kuanza ujenzi kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo naomba nimwelekeze Meneja wa TARURA wa Wilaya hii ya Mbozi kuhakikisha kwamba wanaleta maombi hayo kama ni kipaumbele ili Serikali iweze kufanya tathmini na kuona uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi huo, ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza. Lini Serikali itatenga fedha za kutosha ili barabara inayotoka Mtandika kwenda Ikula iweze kujengwa kwa sababu barabara ile ni hatarishi sana na wakati wa mvua haipitiki wanawake wajawazito wanapandishwa mshikaki kwenda katika kituo cha afya kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii barabara ya kutoka Mtandika kwenda Igula na vijiji ambavyo amevitaja Mheshimiwa Mbunge ni kweli ni barabara muhimu na inapelekea wananchi kufika kwenye kituo cha afya kwa ajili ya huduma za afya. Kwa hivyo Serikali itaendelea kufanya tathmini ya gharama zinazohitajika ili fedha iweze kutafutwa na kuiboresha barabara hiyo ili kipindi cha masika iweze kupitika vizuri na wananchi waweze kupata huduma nzuri za usafiri, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina swali moja la nyongeza. Iliundwa tume ya kuja kuangalia jengo lile la Mtwara tangu mwaka 2020 na tume ile ikapendekeza kwamba jengo lile lisitumike;

Je, ni lini sasa Seriali itaamua kutuletea fedha ili tuweze kupanga sehemu nyingine kwa sababu jengo lile haliko salama sasa kwa wafanyakazi waliopo mule ndani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua kwamba jengo lile ni la siku nyingi na ni chakavu na kwa kweli halina sifa ya kuendelea kutumika kama jengo la halmashauri. Hivyo, Serikali imeweka kipaumbele baada ya kukamilisha majengo haya ambayo mengi yako katika hatua za ukamilishaji katika halmashauri zile mpya, tutakwenda kwenye halmashauri kongwe ikiwepo Halmashauri ya Mtwara Mikindani na nimwakikishie kwamba tutahakikisha kwamba Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa jengo hilo, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kunipa kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga ni halmashauri kongwe na jengo la utawala halijakamilika. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa jengo la utawala Halmashauri ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christina Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilipeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la utawala katika Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Tunafahamu jengo lile halijakamilika, lakini ujenzi huu unakwenda kwa awamu. Awamu ya kwanza fedha zimepelekwa na kazi ya ujenzi imeanza. Nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha ili ipeleke awamu ya pili kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo hilo, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jengo la Halmashauri ya Rungwe ni jengo la muda mrefu sana.

Ni lini Serikali itatupatia fedha angalau kufanya ukarabati na kuongezea baadhi ya vyumba ili kuwawezesha wafanyakazi wafanye kazi vizuri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilitoa maelekezo kwa wakurugenzi wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwamba pamoja na kutegemea fedha kutoka Serikali kuu lakini wanao wajibu wa kutenga fedha kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya ukarabati mdogo mdogo pia kuongeza vyumba viwili, vitatu katika majengo ya utawala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa nina uhakika kwamba Halmashauri ya Rungwe wana uwezo wa kufanya ukarabati wa majengo yale nitumie fursa hii kumwelekeza Mkurugenzi kuanza kuweka kipaumbele kwa awamu kwa ajili ya ukarabati wa majengo ya halmashauri na pia kuongeza vyumba vichache ambavyo vinahitajika, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Natambua Serikali imekuwa ikitenga fedha katika ujenzi wa hospitali wa halmashauri ya Mji wa Bunda. Sasa ningependa kusikia kwa mwaka huu wa fedha nini tamko la Serikali ili hospitali ile iweze kumalizika haraka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa hospitali za halmashauri ikiwemo hospitali ya Halmashauri ya Bunda unakwenda kwa awamu. Kuna awamu ya kwanza ambapo fedha zilipelekwa, awamu ya pili majengo yapo yaliyokamilika na yako ambayo hayajakamilika. Nimhakikishie kwamba Serikali imeweka mpango mkakati wa kuhakikisha inatafuta fedha kwa awamu zinazofuata ili hospitali hizi zote zikamilike na kuwa na miundombinu inayotakiwa kutoa huduma kwa wananchi na hospitali hii ya Bunda pia itapewa kipaumbele.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii, naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza nishukuru Serikali kwa kupeleka fedha katika majengo ya OPD na upasuaji lakini Hospitali ya Mji wa

Bariadi bado ina majengo mengi chakavu ikiwemo jengo la wagonjwa mahututi pia na majengo ya wodi;

Je, Serikali ina mpango gani wa kuyakarabati ili yaweze kutoa huduma bora kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Hospitali ya Mji wa Bariadi ina changamoto ya upungufu wa wauguzi na madaktari; je, Serikali inatoa tamko gani juu ya upungufu huu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Hospitali ya Mji wa Bariadi ni hospitali kongwe na ndiyo maana Serikali iliona umuhimu wa kupeleka shilingi milioni 900 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa majengo ya upasuaji, na jengo la OPD. Zoezi hili la ukarabati na upanuzi wa hospitali ile ni endelevu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kila mara Serikali itakuwa inatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa hospitali kongwe basi Hospitali wa Mji wa Bariadi pia itapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni kweli kumekuwa na upungufu wa watumishi wa sekta ya afya katika Halmashauri wa Mji wa Bariadi. Hata hivyo, mwaka uliopita Serikali ilipeleka watumishi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la kupeleka watumishi kila kibali cha ajira kinapotoka Halmashauri ya Bariadi pia itapewa watumishi hao, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi, naomba niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Matamba kinahudumia Kata tano za Kinyika, Matamba, Mlondwe, Itundu na Mfumbi. Kituo hiki kina zaidi ya miaka 30 hakijakarabatiwa.

Je, ni lini Serikali itakarabati kituo hiki ili kiweze kupata majengo mapya ikiwemo mochwari ambapo wananchi wanatumia Wilaya ya Mlale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Matamba ni cha muda mrefu na ni tegemeo la wananchi kutoka katika kata takribani tano katika Wilaya ya Makete. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imekwishaainisha vituo vya afya vikongwe na chakavu na vyenye upungufu wa miundombinu kwa ajili ya kupeleka fedha kwa awamu kwa ajili ya kukarabati na kuvipanua. Kwa hiyo tutatoa kipaumbele pia katika kituo hiki cha Matamba kwa kadri ya bajeti ambavyo tunakwenda kuipanga; ahsante.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana. Pale katika Jimbo la Kinondoni kwenye Kata ya Kigogo Serikali ilituletea jokofu la kuhifadhia maiti lakini limekaa zaidi ya miaka mitatu sasa bila ya kuweza kujengewa eneo lake ilhali tathmini imeshafanyika;

Je, sasa Serikali imepanga kutoa lini fedha ili nyumba zilizokaribu pale ziweze kufidiwa na jengo lile likaanza kujengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Abbas Tarimba, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Kigogo kilipelekewa jokofu lakini Serikali ilielekeza mara vifaa tiba vinavyofikishwa katika vituo vyetu vianze kutumika mapema iwezekanavyo. Kwa hiyo kwanza nitumie fursa hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni kuhakikisha kwamba wanatenga fedha kwa ajili ya kujenga jengo la kuhifadhia maiti na kuingiza jokofu ili lianze kufanya kazi ya kuhudumia wananchi kama inavyotarajiwa, ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa majibu ya Serikali.

Swali la kwanza; kwa kuwa Kiteto ina upungufu wa walimu karibu 800 ukichanganya shule za msingi na sekondari. Kwa hivyo kama isingekuwa siyo hawa 120 hali ingelikuwa mbaya; je, ni lini ni lini Serikali italeta Sheria ya Ajira hapa tuweke kigezo cha kujitolea iwe ni sababu ya mtu kuajiriwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; ni lini Mheshimiwa Waziri atakuja Kiteto akutane na Walimu hawa wazalendo wanaojitolea wanaojitolea ili azungumze nao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Edward Kisau Olelekaita, Mbunge wa Jimbo la Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Kiteto ina upungufu wa walimu, lakini niwapongeze Halmashauri ya Kiteto kwa kuweka bajeti angalau kidogo kwa ajili Walimu wanaojitolea. Nimhakikishie kwamba Serikali imeweka mpango na mwongozo kwa ajili ya kuwawezesha Walimu wanaojitolea kutambulika rasmi, lakini pia kupewa kipaumbele wakati fursa za ajira zinapojitokeza na kwa kuwa Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan leo kupitia Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ametangaza jumla ya ajira 21,200 za Kada ya Elimu lakini pia na Kada ya Afya, niwatie shime hawa Walimu wanaojitolea Kiteto na maeneo mengine kuomba ajira hizo ili waweze kupewa kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili kuhusiana na kukutana na Walimu hawa sisi tuko tayari baada ya shughuli hizi za Bunge, basi tuambatane na Mheshimiwa Mbunge, ili tuweze kuonana na Walimu hao na kuwatia moyo kufanya kazi nzuri, ahsante.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, pamoja na majibu ya mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; upungufu uliopo katika kila Kituo cha Majengo tuna upungufu huo katika Kituo cha Afya Jinyecha, Kiromba na Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Nanyamba na kupelekea kuwa na upungufu wa watumishi 610; je, Serikali ina mpango gani wa dharura kupunguza tatizo hilo la watumishi katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Wizara ya Afya imetoa mwongozo wa wanachuo wa kada ya afya ambao wamemaliza waweze kujitolea katika vituo vya kutolea huduma.

Je, Serikali haioni sasa ni muda muafaka wa kutenga fedha kiasi ili wahitimu hawa sasa waanze kufanya kazi katika maeneo yenye upungufu mkubwa wa watumishi? Kwa sababu kwanza itasaidiia tatizo la watumishi, lakini pili watakuwa wanatumia ujuzi wao wakati wanasubiri ajira za kudumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Halmashauri ya Nanyamba ina upungufu wa watumishi takribani 610 ambayo Mheshimiwa Mbunge amewataja na Mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi, lakini pia kupeleka watumishi wengi zaidi kwenye maeneo yenye changamoto kubwa zaidi ya watumishi hao kama ilivyo katika Halmashauri ya Nanyamba. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge hasa kwenye hizi ajira ambazo tayari zimetangazwa tutahakikisha halmashauri zote ikiwemo Nanyamba ambazo zina upungufu mkubwa zaidi wa watumishi zinapewa kipaumbele zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, Serikali ni kweli kupitia Wizara ya Afya, lakini pia Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumetoa mwongozo wa namna ya watumishi wa kada za afya kujitolea kwenye vituo vya huduma zetu. Tumeelekeza Wakurugenzi kutenga fedha za angalau posho kwa ajili ya wanaojitolea katika vituo vyetu, niendelee kusisitiza kwamba suala hili ni muhimu Wakurugenzi wafanye hivyo ili kuendelea kupunguza upungufu wa watumishi katika sekta hizo, ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali yanayojaribu kuwafariji wananchi wa Kinyangiri na Mkalama nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kinyangiri ni cha enzi ya ukoloni, ni kituo cha siku nyingi sana na kinahudumia Tarafa nzima, kilipelekea mpaka kiongozi mkubwa wa chama kinachounda Ilani kuwaahidi wananchi wa Kinyangiri kwamba ifikapo Disemba kama hawajapata majengo waandamane ofisini kwake. Serikali na Wizara ina kauli gani kuhusu kauli hii nzito ya Kiongozi mkubwa wa chama kinachounda Ilani?

Swali la pili; Kituo cha Afya Mkalama pia ni cha wakati wa ukoloni hakina uwezo hata wa kufunga P.O.P kama mtu amevunjika mkono au mguu, hivyo wananchi wanateseka na kinahudumia wananchi takribani 15,000. Serikali ina- commitment gani kuhusiana na bajeti hii inayokuja kuhusiana na Kituo hiki cha Afya cha Mkalama? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Kinyangiri ni kituo chakavu na kituo kongwe, Serikali imeshaweka mpango wa kutafuta fedha ili kwenda kukikarabati pia kuongeza majengo ambayo yanapungua. Nimhakikishie kwamba Serikali hii kwa sababu inatekeleza Ilani cha Chama cha Mapinduzi na Kiongozi wetu alifika pale na kutoa maelekezo hayo, tunachukua maelekezo hayo na tunaanza kuyafanyia kazi kuhakikisha tunapata fedha kwa ajili ya kituo cha Kinyangiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Pili; kuhusiana na kituo cha afya cha Mkalama ambacho nacho ni chakavu tutaendelea kutenga fedha kwa awamu ili tuweze kuvikarabati vituo kama hivi pia kuongeza miundombinu ambayo inakosekana. Ahsante.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba niishukuru Serikali kwa majibu mazuri pamoja na kwamba wananchi walitegemea iwe ni hospitali lakini kwa sababu kwa kuwa Halmashauri imeshakuwa na hospitali haiwezekani kupata hospitali nyingine ya Wilaya.

Je, ni lini fedha hizi ambazo zimetengwa zitakwenda kwa ajili ya utekelezaji kwa sababu mwaka wenyewe ndiyo unaelekea mwisho maana Juni ndiyo mwisho.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, naomba Mheshimiwa Waziri aweze kuongozana nami kipindi hiki ambacho Bunge linaendelea aweze kwenda kuona kituo chenyewe cha afya ambacho tunakizungumzia kwa sababu kina hali mbaya sana. Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Sera ya Afya kwa sasa Halmashauri moja inakuwa na hospitali moja na ndiyo maana Serikali ilileta fedha imejenga Hospitali ya Halmashauri, kwa hiyo, hiki lazima kiendelee kama kituo cha afya. Fedha hizi zitapelekwa ndani ya mwaka wa fedha huu wa 2022/2023 Serikali inatafuta fedha ili kupeleka fedha kwa ajili ya mpango huo wa kukamilisha kituo hicho.

Mheshimiwa Spika, niko tayari kuongozana nae na ningeomba uridhie tuongozane baada ya kuahirisha Bunge hili ili tukapate muda wa kutosha, tufanye ziara hiyo na kufanya majukumu hayo. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, aliyekuwa Waziri wa TAMISEMI alituahidi mwaka jana kwamba angetupatia kituo cha afya kwenye Kata ile ya Kirua Vunjo Kusini kwenye Kijiji cha Kohesa. Sijui mtaanza lini kujenga hospitali hiyo kwa sababu tulipata mbadala wa kupata Hospitali ya Wilaya.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi ya Serikali itatekelezwa, ni suala la muda tu kwa hiyo Serikali inatafuta fedha ili kwenda kutekeleza ahadi hiyo kupeleka Kituo cha Afya katika Kata aliyoitaja, ahsante.
MHE. DANIEL S. BARAN: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Kwa kuwa, Kituo cha Afya cha Gallapo kinahudumia Tarafa nzima ya Babati ikiwemo Kata za Endakiso, Mamire, Qash na Gallapo. Je, ni lini Serikali itajenga nyumba ya Mama na Mtoto na chumba cha kuhifadhia maiti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Sillo Baran, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nilifanya ziara Babati Vijijini, tulishirikiana sana na Mheshimiwa Mbunge tulifika Kituo cha Afya cha Gallapo, ni kweli kinahitaji muindombinu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Serikali imeweka mpango wa kutafuta fedha kupeleka Gallapo ili kianze ujenzi wa majengo ya Mama na Mtoto na majengo ambayo yanapungua, ahsante sana.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Kata ya Kimala ipo pembezoni sana mwa Wilaya ya Kilolo na hakuna Kituo cha Afya, katika ile Kata barabara hazipitiki wananchi wanaenda katika Kituo cha Afya cha Dabaga.

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kuwajengea Kituo cha Afya katika Kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata hii ya Kimala ambayo iko pembezoni tulishaelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo kufanya tathmini na kuwasilisha Kata za kipaumbele za kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa vituo cha afya. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Mkurugenzi kufanya hayo maelekezo ya Serikali na kutuletea, ikiwa ni kipaumbele cha Halmashauri hiyo basi Serikali itaona namna ya kutafuta fedha kushirikiana na mapato ya ndani lakini pia fedha za Serikali Kuu kwa ajili ya ujenzi. Ahsante. (Makofi)
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kata ya Endago ya Wilaya ya Hanang ina wakazi zaidi ya 5,600 lakini haijawahi kuwa na Kituo cha Afya wala Zahanati. Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya afya katika Kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kata hii ina idadi kubwa ya wananchi zaidi ya 5,000 lakini haina zahanati. Nimhakikishie kwamba tunaweka mpango wa kutafuta fedha kwenda kujenga zahanati katika eneo lile, ikibidi tunaweza tukaona uwezekano wa kujenga Kituo cha Afya baada ya tathmini kuona inakidhi vigezo. Ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kituo cha Afya Mtina kilichopo katika Jimbo la Tunduru Kusini kilitegewa shilingi milioni 250 katika bajeti hii ambayo ipo 2022/2023. Je, ni lini Serikali itapeleka pesa hii kwa ajili ya kuboresha huduma ya Mama na Watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba kwa sababu ipo kwenye bajeti ya mwaka huu wa fedha, naamini kwamba ifikapo Juni 30, fedha zitakuwa zimepelekwa kwa ajili ya ukamilishaji wa miundombinu hiyo. Ahsante.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wilaya ya Kilindi ina Tarafa Nne, Tarafa Tatu zina vituo vya afya. Je, ni lini Serikali itajenga kituo afya Tarafa ya Kimbe, Kijiji cha Ndegerwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Omari Kigua Mbunge wa Jimbo la Kilindi kama ifiatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Tarafa hii ya Kimbe ambayo haina kituo cha afya tayari ilishawekwa kwenye mpango wa Tarafa za kimkakati, sasa fedha tu inatafutwa ikishapatikana itakwenda kujenga kituo cha afya kwa ajili ya kusogeza huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kituo cha Afya cha Negezi na Mwang’alanga ni moja kati ya vituo vya afya ambavyo vimeanza kufanya kazi katika kipindi hiki lakini bado vina mapungufu ya wodi za kawaida za wagonjwa, mapungufu ya mochwari na walk ways. Ni lini Serikali itakwenda kukamilisha vituo hivi vianze kufanya kazi ipasavyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Negezi na hivyo vingine ambavyo Mheshimiwa Mbunge amevitaja ni miongoni mwa vituo ambavyo Serikali imeweka mpango wa kuhakikisha vinakamilishwa kwanza kabla ya kuanza vituo vingine vipya, ndiyo maana katika mwaka uliopita wa fedha na mwaka huu hatujajenga vituo vingi sana vya afya vipya kwa sababu lengo ni kukamilisha kwanza vituo ambavyo vimeanza kwa sehemu ili vitoe huduma kwa upana wake na baadae tuende kwenye vituo vingine.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ipo kwenye kipaumbele. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninashukuru kwa majibu mazuri lakini kuna changamoto ambayo ipo.

Mheshimiwa Spika, hii barabara tunayoiongelea hapa ni barabara ambayo ni ahadi ya Hayati Mheshimiwa Rais Magufuli na pia kumekuwa na barabara nyingine ya Chapwa, Chindi, Msangano ambayo hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja Songwe tarehe 06 Julai, 2020. Ninataka kufahamu kwa nini ahadi za Viongozi hazitekelezeki kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, kuna changamoto nyingine ambayo ipo ya ujenzi hafifu wa barabara za lami kwa TARURA. Ninataka kufahamu ni kwa nini barabara zao haziwi na ubora, mfano mzuri uko katika Jiji lako la Mbeya utaona barabara ya Kabwe – Isanga, barabara ya Mafiati - Airport, barabara ile ya kutoka njiapanda ya Ilonda kwenda Isyesye ni barabara zinazoharibika kabla ya muda.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu ni kwa nini barabara zao zinakuwa hazina ubora? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa ya Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi zote za Viongozi Wakuu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji wake na Serikali imekuwa ikitekeleza ahadi za viongozi kwa awamu kwa sababu ziko nyingi, kwa hiyo kadri ya fedha zinavyopatikana ahadi zile zinatekelezwa. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba ahadi hii ya Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri Mkuu ni kipaumbele na Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji. Ndiyo maana katika bajeti ijayo itatenga Bilioni Moja na Milioni Mia Tano kwa ajili ya kuanza utekelezaji huo.

Mheshimiwa Spika, kuhusu barabara za lami za TARURA barabara zetu za lami za kipindi cha nyuma kabla ya 2022 zilikuwa zinajengwa kwa maana ya kubeba uzito wa chini ya tani 10 hadi 15, baada ya kuona siyo rahisi ku-control magari yenye uzito mkubwa Serikali kupitia TARURA tumeborsha sasa tunakwenda tani 30 na kuendelea. Kwa hiyo sababu ya kuonekana barabara zile zilikuwa ni dhaifu ni kwa sababu zilikuwa zinajengwa kwa kiwango cha tani 10 lakini magari mazito zaidi yaliweza kupita, tunaamini sasa hatutakuwa na changamoto hiyo kwa sababu tumeboresha mfumo huo. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya kutoka Jimboni kwako Mheshimiwa Waziri Wanging’ombe kuelekea Lupira, kwa maana Kipengere - Lupila na barabara ya Esaprano. Barabara hizi ni za kiuchumi lakini zimekuwa zikisumbua kwa muda mrefu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mbunge jirani yangu amekumbusha suala la msingi na tayari nimhakikishie kwamba kwenye bajeti ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI suala hilo ni kipaumbele kujenga barabara kutoka kipengere kuelekea kule Lupila na itatekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ningependa kujua maana katika Hospitali yetu Kuu ya Wilaya Bomani, jokofu lake limekuwa likiharibika mara kwa mara.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba Jokofu lile linafanya kazi ili watu wapate huduma ambayo inastahili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli jokofu la Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tarime ni la siku nyingi ni chakavu na linaleta usumbufu wa kuharibika mara kwa mara, lakini Serikali imeshatenga fedha katika mwaka wa fedha ujao 2023/2024 kwa ajili ya kununua jokofu lingine kwa ajili ya Hospitali ya Mji wa Tarime. Ahsante.
MHE. JAFARI W CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Vituo vya Afya vitatu kwa maana ya Kinesi, Changunge na Kituo cha Nyamagaro havina chumba cha kuhifadhia maiti. Nataka nijue mpango wa Serikali wa ujenzi wa vyumba hivi kwa ajili ya kunusuru na kusaidia wananchi maeneo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Jimbo la Rorya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba vituo hivi ambavyo vingine ni vipya havina majengo ya kuhifadhia maiti, lakini mpango wa Serikali ni kuendelea kujenga vituo hivi kwa awamu. Tumejenga majengo awamu ya kwanza, tumejenga awamu ya pili na sasa tunakwenda awamu ya tatu kwa ajili ya kujenga majengo mengine yakiwemo majengo haya ya kuhifadhia miili. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali kwamba Mahakama imetupilia mbali suala hili, lakini je, hamuoni sasa iko haja ya Serikali na wananchi tukaweza kukaa pamoja tukapata uelewa wa pamoja ili wajue kwamba kweli walilipwa?

Swali la pili; je, yale maegesho ni lini sasa pataanza kujengwa maana bado pako wazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dorothy Kilave Mbunge wa Jimbo la Temeke kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaona umuhimu wa kukaa na wananchi hawa katika kujenga uelewa wa pamoja ili kuondoa sintofahamu ya baadhi ya wanaodai kufikiri kwamba hawajalipwa. Kwa hiyo nikuhakikishie kwamba tutapanga utaratibu wa kwenda kuonana na wadai hao ili tuweze kuwapa uelewa wa pamoja wajue kwamba tayari walikwisha lipwa haki zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kujua lini ujenzi unaanza, naomba hili tulichukue kama Serikali tukalifanyie kazi tuweze kuona lini ujenzi huu unaanza, ahsante.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, tatizo lililopo ni kwamba, hata wale ambao wameshapata vitambulisho hawapewi huduma inayostahili kadiri ya utaratibu uliopo. Nini kauli ya Serikali kwa hawa ambao wamepata vitambulisho, lakini hawapati huduma ambayo wanastahili?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; lini sasa hawa waliobaki 3,440 nao watapata vitambulisho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika,
naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaelekeza kuhakikisha kila halmashauri kwanza inaandikisha na kuwapa vitambulisho wazee
wote wenye umri wa miaka 60 na kuendelea, wasio na uwezo, lakini inatenga dirisha kwa ajili ya huduma kwa wazee na kuhakikisha kwamba, dawa zote muhimu zinapatikana kwa ajili ya wazee. Kwa hiyo, naomba nitoe Kauli ya Serikali kwamba, wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa wahakikishe maelekezo ya Serikali yanatekelezwa na wazee wetu wapate huduma kama inavyostahiki.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, kuhusu vitambulisho kwa wazee waliobaki, kama nilivyojibu kwenye swali langu la msingi kwamba, mwaka ujao wa fedha Halmashauri watatenga fedha kwa ajili ya kuwapa vitambulisho wazee waliobaki 3440.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa fursa ya maswali madogo ya nyongeza. Kwanza, naishukuru Serikali kwa kukubali ombi hili na nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu aliahidi, wananchi wa Laela wanamshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza la nyongeza; Kata ya Ilemba ina wakazi wapatao 30,000 na ni miaka kumi sasa wanajenga kituo chao cha afya, hakijakamilika: Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga juhudi za wananchi kukamilisha kituo hiki cha afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; Kata ya Msandamuungano kuna kituo cha afya ambacho kinajengo moja tu la OPD; Serikali ina mpango gani wa kuongeza majengo ili kiweze kutoa huduma zote zinazohitajika katika kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata hii ya Ilemba ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge ambayo wananchi wameanza ujenzi wa kituo cha afya; kwanza nitumie fursa hii kuwapongeza wananchi wa Kata hii kwa kuongeza nguvu zao katika ujenzi wa kituo hiki cha afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwahakikishie kwamba Serikali imeweka mpango mzuri wa kuunga nguvu za wananchi katika ukamilishaji wa majengo ya vituo vya afya na zahanati na tutaendelea kutenga bajeti na mara tukiwa na fedha hiyo, tutaona uwezekano pia wa kuchangia kukamilisha hicho kituo cha afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na Jengo la OPD lililopo katika kituo hicho, ni kweli tuna vituo vingi vya afya vyenye majengo machache na vinahitaji kuongezewa majengo mengine, na mpango wa Serikali ni kuendelea kutafuta fedha na kupeleka kwenye majengo haya kikiwemo kituo hiki ili majengo yakamilike na kutoa huduma bora kwa wananchi, ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kituo cha Njombe Mjini ni kituo kongwe katikati ya Mji, kimekuwa na ahadi za muda mrefu: Ni lini sasa kituo hiki kitapanuliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Mwanyika, Mbunge wa Jimbo la Njombe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Njombe Mjini ni kikongwe na ni chakavu, na pia kina miundombinu michache na Serikali imeshafanya tathmini ya uhitaji wa majengo ya ziada na kazi inayoendelea sasa ni kutafuta fedha ili fedha ikipatikana tukaongeze majengo yale na kukiwezesha kile kituo cha afya kufanya kazi inayotarajiwa, ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Wananchi wa Kata ya Narumu wameshatenga eneo kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha afya cha Kata ya Narumu; je, ni lini Serikali itatuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hiki cha Narumu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tuwapongeze wananchi wa Kata ya Narumu kwa ajili ya kutenga eneo kwa ujenzi wa kituo cha afya. Pia niwatie moyo kwamba waanze kwa nguvu zao kujenga kile kituo cha afya na baadaye Serikali ikipata fedha, basi tutakwenda kuwaunga mkono, ahsante. (Makofi)
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali kwa kutambua uwepo wa maboma nchini.

Je, Serikali haioni haja ya kutafuata programu nyingine ya kufanya maboresho katika Ofisi za Kata baada ya programu ya Ruzuku ya Uendelezaji Mitaji Serikali za Mitaa kukoma? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliridhia watendaji walipwe shilingi 100,000; je, Serikali sasa haioni yale malipo yao yakakatwa at source, yakalipwa na Hazina katika mapato ya Halmashauri kwa sababu yanapitia kwenye mfumo wa Treasury Single Account ili kuondokana na usumbufu unaotokana na ucheleweshwaji wa Watendaji wa Kata kupata yale mafao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Ofisi za Maafisa Watendaji za Kata, na pia Ofisi za Watendaji wengine wote wa Serikali katika Halmashauri zetu na ndiyo maana imeendelea kutenga fedha kwa awamu, kuhakikisha kwamba tunakamilisha majengo hayo na fedha hizo ni kupitia mapato ya ndani, na pia kupitia fedha za Serikali Kuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nachukua fursa hii kuwakumbusha na kuwasisitiza Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali Mitaa kote nchini kuweka kipaumbele katika bajeti za mapato ya ndani kwa ajili ya Ujenzi wa Ofisi za Kata na pia Ofisi za Vijiji na Ofisi nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na posho za Maafisa Watendaji wa Kata shilingi 100,000, Serikali ilishatoa maelekezo, na ni wajibu wa Wakurugenzi kuhakikisha fedha za posho za Watendaji wa Kata zinawafikia kwa wakati bila ucheleweshaji wowote. Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutafuatilia kuhakikisha kwamba fedha hizo zinawafikia kwa wakati, ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Swali langu ni kwamba; je, ni lini Serikali itapeleka fedha Wilayani Kilwa kwa ajili ya ujenzi wa ofisi za Maafisa Watendaji Kata wa Kata za Somanga, Namayuni, Mitole na Njinjo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshaelekeza kutumia fedha za mapato ya ndani kuanza Ujenzi wa Ofisi za Maafisa Watendaji wa Kata. Nitumie fursa hii kusisitiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilwa kutenga fedha kwa ajili ya Kata hizi za Somanga na Kata nyingine ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja, ili watendaji wetu wapate maeneo mazuri ya kufanyia kazi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa majibu mazuri ya Serikali; lakini pia naomba niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, changamoto iliyopo hapo Ikungi ni sawa sawa na iliyopo katika Jimbo la Singida Kaskazini katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida ambapo tulisha wasilisha maandiko kwa ajili ya kupatiwa soko la kisasa katika mji wa Melya njia panda ya Melya lakini hadi sasa hakuna kinachoendelea.

Je, Serikali inatoa commitment gani kwa ajili ya kujenga soko hilo la kisasa kwa ajili ya maendeleo ya wananchi?

Swali la pili, Mji wa Ikungi pamoja na Singida Kaskazini hazina stendi zinazoeleweka za kisasa kwa ajili ya magari kuingia na kutoka. Je,Serikali sasa itajenga lini stendi hizo kwa ajili ya kupendezesha miji yetu lakini pia hata kuingizia mapato halmashuri zetu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa
Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Igondo Ramadhani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto hii ambayo pia iko katika Jimbo la Singida Kaskazini Halmashauri ya Singida la kukosa soko, na niwapongeze Halmashauri ya Singida kwa sababu tayari kweli walishawasilisha andiko mkakati kwa ajili ya ujenzi wa soko la kisasa. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wa Ikungi pamoja na Mheshimiwa Mbunge wa Singida Kaskazini kwamba Serikali inaendelea na uchambuzi wa maandiko yale kuona kama yanakidhi vigezo vya kuwa miradi ya kimkakati ili fedha ziweze kutafutwa kwa ajili ya kuwezesha ujenzi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kuhusiana na changamoto ya stendi ya mabasi, Serikali imeshaweka mpango kazi kwenye halmashauri zetu zote kuanza kuainisha maeneo ambayo yanatakiwa kujenga stendi lakini pili kuanza kutenga fedha za mapato ya ndani pamoja na Serikali kuu kutafuta fedha kwa ajili ya kujenga maeneo hayo. Kwa hiyo Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Stendi hizo zinajengwa, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; kwa kuwa uko mradi wa TACTIC wa kujenga soko la kisasa pale Ipembe lakini na soko la vitunguu. Nataka kujua ni lini mradi huu utatekelezwa ili wananchi waweze kupata huduma stahiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sima kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa TATCTIC una awamu tatu. Awamu ya kwanza tayari iko hatua ya kutafuta wakandarasi, awamu ya pili iko hatua ya usanifu wa mwisho na awamu ya tatu itafanyiwa usanifu. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba kabla ya mwaka 2025 Serikali imeweka commitment kuhakikisha kwamba miradi yote ya TACTIC itakuwa imekamilika kwa sehemu na mingi iko kwenye utekelezaji hatua za mwisho, ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mji wa chemba unakuwa kwa kasi lakini hauna soko kabisa. Naomba kujua mkakati wa Serikali wa kujenga soko pale kwenye mji wa Chemba, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Monni Mbunge wa Jimbo la Chemba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nielekeze Mkurugenzi wa halmashauri ya Chemba kuainisha na kuandaa eneo kwa ajili ya ujenzi wa soko na kuleta andiko la kuona uwezo wa halmashauri kwa mapato ya ndani yanafikia eneo gani ili Serikali Kuu iweze kuona sehemu gani inahitaji kuchangia ili kujenga soko katika mji huu wa Chemba, ahsante.
MHE.NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza nashukuru kwa majibu ya Mheshimiwa Waziri.

Swali la kwanza, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia walemavu ambao hawajiwezi kujiunga na vikundi, kuwasaidia angalau baiskeli ya kutembelea?

Swali la pili; je, Mheshimiwa Waziri uko tayari baada ya Bunge hili tuongazane mimi na wewe kwenda kuwatambua walemavu walioko Mbogwe na kuwasikiliza shida zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali wawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga Mbunge wa Jimbo la Mbogwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa au utaratibu wa mikopo ya asilimia kumi kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kundi la watu wenye ulemavu hawalazimiki kujiunga kwenye vikundi, hata mmoja anaweza akakopeshwa mkopo kama yeye na akafanya shughuli zake za ujasiriamali. Tayari wengi wameendelea kupata huduma hiyo kwa kupata mkopo kwa mtu moja mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na viti mwendo kwa watu wenye ulemavu utaratibu wa Serikali upo na maafisa maendeleo ya jamii katika maeneo hayo wanaainisha. Tunahusiana na wadau mbalimbali wanaendelea kuwasaidia. Kwa hiyo nitoe wito kwa halmashauri ya Mbogwe kuwatambua watu wenye ulemavu wanaohitaji viti mwendo ili Serikali iweze kuona namna ya kushirikiana na wadau katika kuwawezesha kupata viti mwendo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge baada ya Bunge hili la bajeti ili twende Mbogwe tuweze kupitia baadhi ya vikundi ambavyo vimenufaika, ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, kwa kuwa Serikali imesimamisha kwa muda utoaji wa mikopo ya asilimia kumi kwa mfumo uliopo mwanzo, na sasa hivi halmashuri hazitoi tena, ni lini serikali inakusudia kuleta hapa mwongozo wa utoaji mikopo hiyo ambao tutaupitia kwa pamoja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa
Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Constantine Kanyasu Mbunge wa Jimbo la Geita Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imesitisha kwa muda utaoji wa mikopo wa asilimia kumi ili kupitia mwongozo vizuri ili kuhakikisha kwamba fedha ambazo zinakopeshwa zinarejeshwa lakini zinakuwa na tija zaidi kwa vikundi ambavyo vinakopeswa. Serikali iko kwenye hatua ya kuupitia mwongozo huo na mara utakapo kuwa tayari Waheshimiwa Wabunge wataufahamu.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri ya kuahidi kuleta magari mawili kwenye hivi vituo viwili cha Mtwango pamoja na cha Mgololo. Swali langu la nyongeza ni moja.

Je, kwa kuwa wananchi katika maeneo haya wameonesha jitihada kubwa za kuanza kujenga vituo hivyo vya afya, Serikali iko tayari kuleta fedha ili vikamilike mara moja kutokana na uhitaji mkubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge amewasilisha hoja hizi za Vituo vya Afya vya Mtwango na Mgololo. Niwapongeze wananchi wa Jimbo la Mufindi Kusini kwa kuanza kujitolea nguvu zao. Nawahakikishia kwamba Serikali imeshaweka kwenye mpango wa kupeleka fedha ili kukamilisha vituo hivi vianze kutoa huduma kwa wananchi, ahsante.
MHE ALLY M. KASINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Nanjilinji ambayo ina umbali wa zaidi ya kilomita 100 kutoka sehemu ya kutolea huduma ya afya kwa maana ya Hospitali ya Wilaya pale Kinyonga haina gari la wagonjwa.

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kupeleka gari la wagonjwa kwa ajili ya Kituo cha Afya Nanjirinji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Kassinge, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliahidi kupeleka gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Nanjirinji na nimhakikishie kwamba kwenye magari ambayo tayari yameanza kununuliwa, tayari magari 117 yameingia kati ya 316 na kituo hiki kitapewa kipaumbele kupewa gari la wagonjwa, ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Katika Halmashauri yetu ya Wilaya ya Kilwa ina majimbo mawili; je, Serikali ina mpango gani wa kuleta ambulance zaidi ya moja ili kukidhi uhitaji katika Wilaya yetu ya Kilwa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kusini, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunapeleka magari ya wagonjwa kwenye kila halmashauri, lakini ndani ya halmashauri kuna vipaumbele vya maeneo ambayo yana uhitaji mkubwa zaidi wa magari ya wagonjwa. Kwa hiyo, tunapeleka magari mawili katika Halmashauri ya Kilwa, lakini pia kukiwa na uhitaji na vigezo vya kutosha, basi tutaona namna ya kuepeleka gari nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Jimbo la Buchosa lina idadi ya watu wasiopungua 400,000 na vituo vya afya vinane, lakini lina gari la wagonjwa moja na watu wengi wanaishi visiwani. Je, Serikali iko tayari sasa kutamka kwamba Jimbo la Buchosa litapata magari ya wagonjwa katika miongoni mwa magari haya ya wagonjwa yanayotolewa na moja lipelekwe visiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba katika magari 316 ya wagonjwa, Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa pia itapelekewa magari mawili ya wagonjwa, ahsante sana.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; hospitali hii ni ya siku nyingi sana na majengo yake yamechakaa sana kiasi kwamba mengine yatalazimika kuvunjwa na kujengwa upya, lakini pia kuna changamoto ya eneo. Kwa Hiyo tunaona kwamba ni busara kuanza sasa kuwaza kwenda kujenga majengo ya ghorofa.

Je, Serikali pamoja na kwamba imetupatia shilingi milioni 900 ambazo tunashukuru sana, je, Serikali haioni kuwa ni muhimu kujipanga kwa ajili ya kujenga maghorofa kwa maana ya kwamba fedha ziongezwe? Hilo moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; hospitali hii haina
mortuary siku zote tangu imejengwa. Tumejitahidi tumejenga mortuary pale na mpaka sasa haijapata majokofu. Je, ni lini Serikali itatupatia majokofu ili ile mortuary ianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli hospitali hii ni kongwe, ni ya siku nyingi na mwezi mmoja uliopita nilifanya ziara pale nikishirikiana na Mheshimiwa Mbunge, lakini tulikubaliana kwamba kwa sababu imekwishaingizwa kwenye Mpango wa Hospitali Kongwe 31 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi ndio maana mwaka wa fedha 2023/2024 imetengewa Milioni 900. Sasa dhamira ya kujenga hospitali mpya ndani ya halmashauri wanaweza wakakaa na kuleta mapendekezo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili na sisi tuweze kuyatathimini na kuona kama yanaweza kutekelezeka ama vinginevyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, niwapongeze kwa kujenga jengo la kuhifadhia miili ya marehemu (mortuary) lakini jokofu liko ndani ya uwezo wa halmashauri kupitia Bohari ya Dawa (MSD). Kwa hiyo, nielekeze Mkurugenzi wa Halmashauri hii kuhakikisha kwamba wanaomba jokofu Kupitia akaunti ya MSD ili waweze kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. JUDITH S. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Serikali iliahidi kwamba imetenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga ambayo miundombinu yake imechakaa sana na ni hospitali ya siku nyingi. Je, ni lini ukarabati huo utaanza ili wananchi wa Wilaya ya Mbinga wapate huduma za afya bora na stahiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Judith Kapinga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bajeti ya Serikali ya 2023/2024 iliyopitishwa hapa Bungeni wiki iliyopita, Serikali imetenga Shilingi Milioni 900 kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali Kongwe ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Je, ni lini sasa Serikali itajenga mortuary katika Kituo cha Malawi kilichopo Yombo Vituka Jimboni Temeke?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatvyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa uwezo wa mapato ya ndani ya Manispaa ya Temeke, naelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke kuweka kipaumbele cha kujenga jengo la kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya cha Yombo Vituka, ahsante.
MHE: YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha Afya cha Eshkesh kilipewa Shilingi Milioni 400 na imekamilisha jengo la OPD na nyumba ya Daktari, lakini bado jengo la Mama na Mtoto na kituo hicho hakijaanza kufanya kazi. Je, sasa ni lini Serikali itakamilisha jengo la Mama na Mtoto ili kituo hicho kianze kufanya kazi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Eshkesh kilipata shilingi milioni 400 na hatua za ujenzi zimefikia umaliziaji wa baadhi ya majengo na ni kweli kwamba jengo la Mama na Mtoto halijakamilika. Nimhakikishie tu kwamba Serikali iliweka mpango wa ujenzi wa vituo vya afya hivi kwa awamu. Tumekwenda awamu ya kwanza tumekamilisha majengo hayo, tunakwenda awamu ya pili kutafuta fedha kwa ajili kukamilisha pia jengo la Mama na Mtoto ili ianze kutoa huduma kwa wananchi, ahsante.
MHE. SELEMAN J. ZEDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Tangu mashine hii ya Ultrasound ifungwe pale Bukene, hakujawahi kuwa na mtaalam wa hii mashine, na kwa hiyo, wagonjwa wanapofika pale hawapati huduma hii, na badala yake wanapelekwa Kituo cha Afya cha Itobo kilichopo zaidi ya kilometa 20: Je, Serikali inaweza kutoa maelekezo maalum kwa Mganga Mkuu wa Halmashauri au Wizarani ili mtaalam wa Ultrasound apelekwe, awe station pale kwa sababu hakuna tija yoyote kuwa na mashine ya Ultrasound wakati mtaalam wa kuiendesha hayupo na, kwa hiyo haifanyi kazi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kwa kuwa jengo mahususi kwa ajili ya kuweka mashine ya X-Ray katika Kituo cha Afya cha Itobo linakamilika; je, ni nini commitment ya Serikali sasa ya kuweka mashine hiyo mara tu jengo hilo litakapokamilika pale Kituo cha Afya cha Itobo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Suleman Jumanne Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali imepeleka mashine ya Ultrasound katika Kituo cha Afya hiki cha Bukene, lakini safari ni hatua. Tulianza kwanza kuandaa mazingira kwa maana ya kandaa majengo na kupeleka mashine. Sasa hatua inayofuata ni kupeleka mtaalam wa mashine ya Ultrasound ili aanze kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumeshatoa maelekezo. Nitumie fursa hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nzenga kuangalia ndani ya wilaya kufanya internal redistribution ya staff kwa ajili ya kwenda kutoa huduma ya Ultrasound, na Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutaangalia uwezekano wa kupata mtaalam mwingine kwa ajili ya kwenda kuongeza nguvu kule Bukene.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhusiana na Jengo la X-Ray katika Kituo cha Afya cha Itobo, ni kweli Serikali inaendelea na ujenzi na mara baada ya kukamilika jengo lile, mashine ya X- Ray itapelekwa ili tuendelee kutoa huduma kwa wananchi wa Itobo, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kituo cha Afya Mlalo ni miongoni mwa vituo vikongwe kabisa ambavyo havina huduma ya X-Ray: Je, ni lini Serikali itahakikisha sasa kituo hiki kinapata huduma hiyo ya X-Ray kwa sababu kinahudumia zaidi ya kata tisa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, vituo vyetu vyote vya afya kote nchini vimewekwa kwenye mpango mkakati wa kujenga majengo kwa ajili ya huduma za upimaji na huduma za X-Ray na Ultrasound zikiwemo. Kwa hiyo, naomba nilichukue hili ili tuweze kufanya tathmini kwenye Kituo hiki cha Afya cha Mlalo tuone uwezekano wa kupata fedha kwa ajili ya kujenga Jengo la X-Ray na baadaye kuweka mashine kwa ajili ya kuendelea kutoa huduma, ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa kuwa uboreshaji huu ni kazi ambayo imepangwa (planned activity): Je, Serikali imepanga kukamilisha lini hii kazi ya uboreshaji wa maeneo ambayo iliyaanzisha?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili: Jimbo la Busanda lina wananchi takribani zaidi ya 700,000; ina kata 22, lakini ina tarafa mbili tu: Ni lini Serikali itaongeza idadi ya tarafa ili wananchi waweze kufikiwa kwa urahisi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, uboreshaji wa miundombinu katika Halmashauri zetu ni zoezi ambalo sasa linaendelea na Serikali imeshajenga majengo mapya ya Halmashauri zaidi ya 115 na inaendelea na ujenzi wa majengo ya Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, na pia tutakwenda kwenye ngazi za kata. Kwa hiyo, zoezi hili ambalo linaendelea kutekelezwa ni la muda, na mara litakapokamilika kutokana na upatikanaji wa fedha, basi tutakwenda kwenye hatua nyingine ya kuona uwezekano wa kuanzisha mamlaka nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuhusiana na kuanzisha tarafa katika Jimbo hili la Busanda, namwomba Mheshimiwa Mbunge na pia nielekeze Halmashauri kufuata taratibu za uanzishwaji wa tarafa, kwa maana ya kufanya vikao kwenye ngazi ya DCC, RCC na kuwasilisha kwenye Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tathmini ifanyike na hatua stahiki ziweze kuchukuliwa, ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Vikao vya DCC na RCC wakati mwingine majibu yake yanachelewa kutoka Serikalini: Je, ni lini Serikali itatupatia majibu ya mabadiliko ya jina la Mji wa Mugumu kuwa Mji wa Serengeti kama lilivyopitishwa na vikao vya DCC na RCC? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amsabi Mrimi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetoa maelekezo na utaratibu wa taarifa na maamuzi na mapendekezo ya DCC na RCC kuletwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI yako wazi. Nisisitize kwamba baada ya vikao hivyo, Makatibu Tawala wa Mikoa wahakikishe kwamba taarifa zinafika Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu jina la Mugumu kwenda kuwa Serengeti, naomba tulichukue hili tukatazame limefikia hatua gani, tuone maoni ya wadau na baadaye Serikali itatoa maamuzi lipi linakwenda kufanyika? Ahsante sana.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza: Kwa kuwa kituo hicho cha Kizazi kilianza kujengwa kwa nguvu za wananchi tangu 2019, mpaka sasa ni miaka mitano; na ninaishukuru Serikali kwa kutenga fedha hizo, lakini mpaka sasa hazijaanza kwenda; nataka Serikali inihakikishie: Je, ni lini kituo hicho kitakamilika ili wananchi waanze kupata huduma katika kituo hicho? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Katika Halmashauri ya Kasulu DC, ipo zahanati katika Kata ya Kagerankanda, zahanati ya Uvinza ina watumishi wawili tu, tena wanaume: Je, ni lini Serikali itamwagiza Mganga Mkuu pamoja na Mkurugenzi kupeleka watumishi wa kile katika zahanati hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niitumie fursa hii kuwapongeza wananchi wa Kibondo kwa kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa kituo cha afya na ndiyo maana Serikali imetambua nguvu zao na kuweza kutenga shilingi milioni 500 ambayo itapelekwa ndani ya mwaka huu wa fedha; na mara baada ya fedha hizo kupelekwa, tunawapa maelekezo ya ndani ya miezi sita kituo cha afya kiwe kimekamilika, wananchi waanze kupata huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusu Zahanati ya Uvinza katika Halmashauri ya Kasulu DC ambayo ina watumishi wawili wa kiume, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tumelichukua hilo, tutalifanyia kazi, lakini Serikali imeendelea kuajiri watumishi. Niseme, katika kipindi cha miaka miwili cha uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan watumishi wa afya 17,000 wameajiriwa na kupelekwa kwenye vituo vyetu na zoezi hilo litaendelea kwa kadri ya upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa kujenga vituo vingi vya afya katika mkoa wangu wa Arusha na vyenye ubora wa hali ya juu, lakini changamoto kubwa ni vifaa tiba ikiwemo na kichomeataka hali inayopelekea akina mama wengi kukosa huduma ya kujifungua: Nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Catherine Magige, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, napokea pongezi hizi za kazi nzuri ya Serikali. Nimhakikishie kwamba fedha za ununuzi wa vifaa tiba zimeendelea kutolewa na vifaa tiba vimesambazwa kwenye vituo, na pia mwaka huu wa fedha fedha zimetengwa kwa ajili ya vifaa tiba. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba zahanati hii itapewa kipaumbele pamoja na ujenzi wa incinerator, ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kituo cha Afya cha Makorongo kimeanza kutumika, lakini baadhi ya majengo hayajakamilika. Mfano, jengo la maabara. Nini kauli ya Serikali ya kukamilisha ujenzi huu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kituo kile kimeanza kutoa huduma za afya lakini jengo la maabara na baadhi ya majengo hayajakamilika na ujenzi huu tunakwenda kwa awamu. Nikuhakikishie kwamba Serikali inatafuta fedha kupitia mapato ya ndani lakini pia kupitia Serikali kuu ili kukamilisha majengo haya, kituo kiweze kutoa huduma vizuri zaidi, ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kituo cha Afya cha Nobola kilichopo katika Tarafa ya Negezi, kimejengwa miaka mingi miaka ya 1970 na kituo hiki kimechakaa sana: Nini mpango wa Serikali wa kukarabati kituo hiki ikiwa ni pamoja na kufanya upanuzi kwa ajili ya kituo hiki? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya vituo vyote vya afya, hospitali kongwe na kuweka mpango kazi wa ukarabati kila mwaka wa fedha. Ndiyo maana katika mwaka huu wa fedha pia katika bajeti yetu tuna fedha kwa ajili ya ukarabati wa vituo hivi vikongwe. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaelekeza Halmashauri ya Kishapu kuleta taarifa ili timu iweze kufanya tathmini na kuona mahitaji ya ukarabati na upanuzi wa kituo hicho, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, Serikali iko tayari kujua sababu za kwa nini Kituo cha Afya cha Iramba Ndogo hakijakamilika ili kiweze kuchukua hatua na kunufaisha wananchi kama ilivyokusudiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kufanya tathmini na kujua sababu zilizopelekea kituo hiki cha afya kutokamilika. Pia itachukua hatua za kisheria na za kinidhamu ikithibitika kuna baadhi ya watumishi ambao hawakufuata taratibu za fedha na kusababisha kituo kutokamilika, ahsante.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kituo cha Afya cha Kata ya Ifumbo ni kituo cha afya cha muda mrefu na kinajengwa kupitia mapato ya ndani ya halmashauri. Je, ni lini Serikali itatoa fedha ya kituo hiki kiweze kukamilika na Wananchi wa Ifumbo waweze kunufaika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masache Kasaka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina utaratibu wa ujenzi wa vituo vya afya kwa kutumia nguvu za wananchi. Niwapongeze Wananchi wa Kituo cha Afya cha Ifumbo lakini tunaendelea kusisitiza kwamba kupitia mapato ya ndani watenge ile asilimia 20, 40 na 60 kwa ajili ya kukamilisha vituo hivi. Endapo halmashauri haina uwezo huo walete andiko hilo ili Serikali iweze kuchangia fedha kwa ajili ya kukamilisha kituo hicho, ahsante.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru. Kata ya Kakola kwenye Jimbo la Tabora Mjini ina jengo la mama na mtoto kwenye zahanati yao. Serikali ina mpango gani wa kumalizia boma hili ili kunusuru afya ya mama na mtoto katika Manispaa ya Tabora? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora kutenga fedha kwa ajili ya kukamilsha boma hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amekuwa mara kwa mara analifuatilia. Fedha inayohitajika ni kidogo iko ndani ya uwezo wa halmashauri na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutafuatilia, ahsante. (Makofi)
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Wananchi wa Vijiji wa Mganzi, Chagana, Nguvumoja, Ilogelo na Mwagala, Jimbo la Igunga wamekamilisha ujenzi wa maboma ya zahanati; je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi kuunga nguvu za wananchi mkono? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nicholaus Ngassa, Mbunge wa Jimbo la Igunga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na ukamilishaji wa maboma ya zahanati yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi lakini ukamilishaji unaenda kwa awamu. Tumeshafanya katika miaka miwili, mitatu yote ya fedha na tutaendelea kufanya hivyo kwa kutumia fedha za mapato ya ndani lakini pia kutumia fedha za Serikali Kuu, ahsante.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Pamoja na majibu haya ya Serikali. Nina maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa soko hili pamoja na stendi ni hitaji kubwa la Wananchi wa Singida Kaskazini. Je, ni lini hasa Serikali itakamilisha hiyo tathmini ili kuweza sasa kutoa nafasi kwa miradi hii kuanza kutekelezeka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa halmashauri imeanza kutenga fedha kidogo kidogo lakini hazitoshi. Je, Serikali sasa ina mkakati gani mahsusi ya kuhakikisha inatumia vyanzo vingine vya fedha kuhakikisha ina supplement ili kukamilisha miradi hii kwa wakati? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba soko na stendi hii ni hitaji kubwa la wananchi na Serikali inatambua hili na ndio maana imeelekeza ifanyike tathmini. Tumewaalekeza Halmashauri hii ya Singida ihakikishe inakamilisha tathmini ndani ya miezi mitatu na kuleta maandiko hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili yaweze kupitiwa na kufanyiwa maamuzi.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali itatenga fedha baada ya kufanya tathmini, itatenga fedha kwa ajili ya kuongeza nguvu za kukamilisha ujenzi wa stendi lakini pia soko ambalo linahitajika, ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kufahamu ni lini Serikali itatujengea soko pamoja na Stendi ya Mkoa wa Songwe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba Mkoa wa Songwe ni miongoni mwa mikoa mipya, hauna stendi lakini na soko na suala hili limekuwa likiulizwa mara kwa mara na Serikali imeendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi na soko katika Mkoa wa Songwe. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ipo kazini na itatekeleza suala hilo, ahsante.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itajenga Soko la Haydom na stendi yake na bahati nzuri Mheshimiwa Naibu Waziri ulifika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Jimbo la Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tulielekeza Halmashauri ya Mbulu Vijijini kufanya tathmini na kuanza kutenga fedha za mapato ya ndani kwa awamu kwa ajili ya ujenzi wa Soko la Haydom. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kusisitiza maelekezo hayo yafanyiwe kazi na pale itakapohitajika nguvu ya Serikali Kuu basi tutakwenda kuunga mkono juhudi za ujenzi wa soko hilo, ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona, je, ni lini Mradi wa TACTIC utaanza ili soko na stendi vijengwe Bukoba Mjini? Hili swali nimeshaliuliza zaidi ya mara tatu ndani ya Bunge hili, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtoe shaka Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeanza utekelezaji wa Mradi wa TACTIC kwa awamu ya kwanza lakini awamu ya pili pia tathmini zinaendelea na awamu ya tatu itakwenda kutekelezwa. Kwa hiyo, Halmashauri ya Bukoba pia ipo katika moja ya awamu hizi na mradi huu utatekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme sijaridhika na jibu la Serikali.

Mheshimiwa Spika, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; hivi Serikali ina mkakati gani haswa wa kuwatumia ma- engineer waliobobea, ma-engineer wa TANROADS, ma-engineer wa TARURA kufanya kazi ya kutatua hili tatizo ambalo ni kubwa sana kwa nchi?

Mheshimiwa Spika, pili; pesa zilizotumika ni nyingi mno kujenga barabara Mkoa wa Dar es Salaam, kujenga barabara kutoka airport kuja Dar es Salaam lakini maji yanayotuama yanaharibu kabisa sura ya Dar es Salaam. Serikali mnatuambia nini leo kitu cha uhakika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mama yangu, Mheshimiwa Anne Kilango Malecela kwamba Serikali kwa kiasi kikubwa ukiangalia kasi ya mafuriko ya barabarani; kwa mfano nenda Tandale, nenda Sinza, nenda maeneo mengi ya Kigogo, Waheshimiwa Wabunge wa Dar es Salaam ni mashahidi, siku za nyuma kulikuwa na mafuriko mengi sana kulikuwa hakukaliki lakini kwa sasa kuna improvement kubwa sana baada ya Mradi wa DMDP na kazi hii inaendelea.

Mheshimiwa Spika, sasa kuhusiana na mkakati wa kuwatumia ma-engineer wabobevu wa TANROADS na TARURA hicho ndicho ambacho Serikali inafanya. Kabla ya ujezi wa mifereji na kingo za mito, engineer hawa wabobevu wanafanya tathmini na kutengeneza ramani na michoro na kazi hizi zinafanyika.

Mheshimiwa Spika, pia, ni kweli bado kuna changamoto kwenye barabara zetu za Jiji la Dar es Salaam kujaa maji mvua zikinyesha na ni suala endelevu ambalo inatakiwa Serikali iendelee kutenga fedha na kuendelea kwa hatua ya kujenga. Nimuhakikishie Mheshimiwa Kilango Malecela kwamba Serikali itaendelea kufanya kazi hiyo, ahsante.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kwa mujibu wa swali hili ni kwamba maji pia hutuama katika barabara za lami ambazo nyingi zinakuwa na mashimo na hata zikitengenezwa mashimo yanajirudia pale pale.

Je, Serikali haioni kwamba sasa ni muhimu kuwa na kitengo katika moja ya halmashauri za Jiji za Dar es Salaam kusimamia utengenezaji wa mashimo yale badala ya kutegemea kandarasi ambazo zikifanya kazi bado mashimo yanatokea tena? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Abbas Tarimba, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ina kitengo tayari cha usimamizi wa matengenezo ya mara kwa mara ya barabara zetu, yakiwemo haya mashimo ambayo yanasababisha maji kutuama. Vitengo hivyo ni Idara za Wakuu wa Idara, kwanza tuna TARURA kila halmashauri ya wilaya, pia tuna ngazi ya mkoa lakini pia kwenye halmashauri kuna ma-engineer. Kwa hiyo, wale ndio wataalamu na vitengo vile ni sahihi kusimamia.

Mheshimiwa Spika, kinachokosekana mara nyingine ni uthabiti na umakini wa usimamizi kwa vile vitengo ambavyo vina ma-engineer tayari. Sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutaendelea kusimamia kwa karibu na kuchukua hatua kwa wale ma-engineer ambao hawatimizi majukumu yao ipasavyo, ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Miradi hiyo iliyotajwa hapo ni kwa ajili ya uboreshaji wa stendi za majiji na manispaa na kwa kuwa halmashauri ninazoziongelea haziangukii kwenye majiji wala manispaa. Je, Serikali inampango gani wa makusudi sasa kuhakikisha wanakwenda kuboresha stendi kwenye Halmashauri zetu za Wilaya ya Mkinga, Pangani, Muheza, Lushoto pamoja na Kilindi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa maeneo ya stendi pia ni moja ya chanzo cha uzalishaji wa ajira hasa kwa kina mama na vijana. Je, Serikali sasa ina mkakati gani wa kuhakikisha miundombinu ya stendi inakuwa rafiki kwa wajasiliamali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa viti maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja ni kweli hazipo kwenye category ya majiji na manispaa na halmashauri hizi kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi, kwamba tutaendelea kutenga fedha kupitia mapato ya ndani lakini pia kupitia Serikali kuu kwa awamu kuhakikisha kwamba stendi hizo zinajengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba halmashauri hizo pia zipo kwenye mpango, tutaendelea kujenga kwa awamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusiana na miundombinu inayowezesha wafanya biashara. Serikali imekuwa ikijenga stendi, inajenga maeneo kwa ajili ya mama lishe na baba lishe, inajenga maeneo ambayo yanaweza ku–accomodate Machinga na wafanyabiashara wadogowadogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo suala hili litaendelea kutekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, swali langu la kwanza, kwenye Wilaya ya Kyerwa tunayo maboma ambayo yanazidi ya miaka 10 mpaka 15. Kwa mfano Kata ya Kimuli kuna boma ambalo linazaidi ya miaka 15 halijakamilishwa na ni nguvu ya wananchi. Kata ya Kikukuru kuna Zahanati ya Omkutembe na yenyewe haijakamilika zaidi ya miaka 10. Je, ni lini Serikali itakamilisha maboma haya ili wananchi waweze kupata huduma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bilakwate, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ukamililishaji wa maboma ambayo yameanza kujengwa kwa nguvu za wananchi nchini kote na mpaka mwezi Juni mwaka huu jumla maboma elfu moja na sitini na sita Serikali ilikuwa imepeleka fedha yamekamilishwa ujenzi wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili linaendelea kwa awamu. Kwa hiyo, ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba maboma haya ya zahanati yenye umri mrefu wa miaka 10 na zaidi yatapewa kipaumbele kwenye bajeti za Serikali. Pia naelekeza kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, kwamba Halmashauri hii ya kyerwa watenge pia mapato ya ndani kuhakikisha wanakamilisha majengo haya kwa huduma za wananchi, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kituo cha Afya Kiloleni Wilaya ya Busega hakina wodi za kulaza wagonjwa, wodi ya wanaume, wanawake na watoto. Je, ni lini Serikali itajenga wodi hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa viti maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kituo cha Afya cha Kiloleni katika Halmashauri ya Busega hakina wodi za kulaza wagonjwa. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, kwamba vituo hivi vya afya vinajengwa kwa awamu. Tunaanza na awamu ya kwanza ya majengo ya OPD, Maabara lakini pia majengo ya mama na mtoto na majengo ya upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua zinazofuata ni kukamilisha kujenga mawodi na miundombinu mingine. Kwa hiyo, ni mhakikishie Mheshimiwa Mbunge, muda huo utakapofika tutahakikisha pia tunatafuta fedha kwa ajili ya kituo hiki cha afya cha Kiloleni, ahsante. (Makofi)
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Halmashauri ya Busekelo wananchi wamejenga maboma kwa ajili ya vituo vya afya, maboma manne. Ikiwa ni Kata ya Lufilyo, Kisegese, Mpombo na Kambasegela. Je, ni lini Serikali itaunga juhudi za wananchi hao kukamilisha maboma hayo ya vituo vya afya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Suma Fyandomo, Mbunge wa viti maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze wananchi wa Jimbo la Busekelo kwa kutoa nguvu zao kuanzisha ujenzi wa maboma ya vituo vya afya, lakini niwahakikishie tu kwamba, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha vituo vya afya kwenye kata za kimkakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakwenda kufanya tathimini kuona kati ya hayo maboma lipi ni lakimkakati ili Serikali itafute fedha kwa ajili ya kuwaunga mkono kukamilisha maboma hayo, ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali la nyongeza. Serikali ilitoa fedha kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Kabwe, lakini mpaka leo kile kituo hakijakamilika kwa sababu fedha hazitoshi. Ni mkakati upi wa Serikali wa kumalizia kituo kile cha afya ili wananchi wa Kabwe wapate huduma pamoja na kata ya jirani ya Korongwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kituo cha afya cha Kabwe kilipelekewa fedha na Serikali kwa ajili ya ujenzi na kwa taarifa kwamba hakijakamilika tutakwenda kwanza kujifunza kwa nini fedha iliyopelekwa haijakamilisha majengo. Kama kuna matumizi mabaya ya fedha ya Serikali wanaohusika watakaothibitika tutachukua hatua za kisheria na za kinidhamu. Lakini pia tutatafuta pia fedha kuhakikisha kwamba kituo kinakamilika na kuanza kutoa huduma kwa wananchi.
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, ninayo maswali ya nyongeza. Kwa kuwa changamoto ya mikopo ya vikundi imekuwa kubwa sana katika maeneo ya Jiji la Dar es salaam na hususani katika Jimbo la Kinondoni, kutokana na masharti mbalimbali wanayopewa wakopaji wanashindwa kukopa. Je, Serikali haioni haja katika hiyo mikakati yake sasa kuangalia sehemu ya mtu kukopa mmoja mmoja?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa wakinamama wengi wajasiliamali wa mitaani wanashindwa kuungana kwenye vikundi na wanahitaji kupata mikopo mmoja mmoja mwenye kuuza mandazi, vitumbua na nini. Je, Serikali imejipanga vipi sasa katika hiyo mikakati yake kuhakikisha kwamba, sasa wanaruhusiwa kukopa mtu mmoja mmoja ili aendeleze biashara yake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza ifahamike kwamba vikundi katika mikopo ya asilimia 10 vinatumika kama dhamana, kwa sababu wajasiliamali wanaokopeshwa kwa mikopo ya asilimia 10 ni wale ambao hawana uwezo wa kutosha kuwa na dhamana ya kupewa mkopo. Kwa hiyo, concept ilikuwa kwamba kikundi ni dhamana.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niseme tumechukua hoja hii na chini ya Mheshimiwa Waziri wetu wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutaifanyia tathimini kwenye tathimini inayoendelea nakuona uwezekano wakuiboresha kama itakuwa inatija, ahsante. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Vijana wengi wa Dar es salaam wanaendesha bodaboda za mikataba. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka kushirikiana na ma-bank yanayotoa mikopo ya bodaboda bank ya NMB na bank ya CRDB ili wanapofungua sasa dirisha la mikopo hii ya asilimia 4:4:2 za vijana, wanawake waweze kutoa mikopo ya vijana kuwakwamua kwenye unyonyaji wa mikataba hii ya bodaboda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Jimbo la Ukonga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema utaratibu wa ukopeshaji wa asilimia 10 unafanyiwa kazi na utaboreshwa, kwa hivyo tutaona pia uwezekano wakuchukua wazo hili na kuliboresha kuona namna ambavyo utawezesha vijana kupata mikopo kwa urahisi zaidi kwa kadri ambavyo itaonekana inawezekana, ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa maelezo mazuri ya Serikali na niipongeze Serikali kwa kweli dawa zipo kwenye vituo vyetu na wananchi wanapata dawa. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, ni nini mkakati madhubuti wa Serikali kuhakikisha kuwa dawa hizi zinazopatikana sasa hivi ziendelee kupatikana katika vituo vya afya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tupate ufafanuzi wa utaratibu uliowekwa pale mgonjwa anapokosa dawa katika hospitali na duka linalomilikiwa na hospitali ili sasa apate dawa kwa ajili ya tiba inayohusiana na matibabu yake, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT FESTO J. DUGANGE) K.n.y. WAZIRI WA AFYA: Mhehimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mkakati wa kuhakikisha kwamba baadhi ya dawa ambazo zinakosekana zinapatikana, moja, tumeelekeza na kusisitiza vituo vyote vya Serikali vifungue maduka ya dawa. Mbali na dispensing za hospitali zenyewe lakini wafungue maduka ya dawa ndani ya hospitali zenyewe, na wahakikishe yale maduka yana dawa zote zilizopo katika ngazi ya kituo husika; ili mgonjwa akikosa dawa pale dispensing aweze kuwa-referred ndani ya hospitali kwenda kuchukua dawa kwenye duka la dawa la hospitali. Kwenye mkakati huo tumeweka kwamba dawa zote lazima zipatikane kwenye duka, ikiwa ni alternative ya filling kutoka dispensing.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, utaratibu ni kwamba mara mgonjwa akiandikiwa cheti cha dawa na kwenda dirisha la dawa kupata dawa zile akapata chache na moja kakosa anaandikiwa cheti kidogo kwa ajili ya kwenda kwenye duka la dawa na kupata dawa zile; na tutaendelea kusimamia utaratibu huo.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri ametuambia kwamba wanatarajia kukamilisha mchakato wa zabuni mwezi Disemba, 2023.

Je, anaweza akatueleza leo kwamba ni lini wana mpango wa kutangaza tenda hii? Maana ili mchakato ukamilike lazima tenda iwe imetangazwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza; Mradi huu wa TACTIC mpaka sasa ulishatangaza tender kwa ajili ya kujenga barabara za lami za Engo Sheraton, Olasiti pamoja na Oljoro ambapo tunakwenda kujenga stendi. Tender ilitangazwa tarehe 27 mwezi Februari, na deadline ilikuwa ni tarehe 14 mwezi wa Nne. Leo miezi mitano imeshapita lakini mkandarasi bado hajakwenda site.

Je, ni lini watampeleka mkandarasi site ili barabara hizi za lami za Engo Sheraton, Olasiti na Oljoro zianze kujengwa mara moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza lini tunatangaza tenda hiyo; kama nilivyosema tupo kwenye hatua za utaratibu wa manunuzi na siwezi kuwa certain sana kusema lini exactily lakini nakuhakikishia tu kwamba by Disemba mwaka huu tutakuwa tumekamilisha taratibu zote za manunuzi, na mkandarasi kwenda site kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na hii tenda ya ujenzi wa barabara hizi ambazo mpaka sasa zaidi ya miezi minne, mitano mkandarasi hajaenda site. Naomba nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, TAMISEMI, kutoa maelekezo kwa Meneja wa TARURA Mkoa wa Arusha, lakini pia Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, kwa maana ya Jiji la Arusha, kuhakikisha wanamfuatilia mzabuni huyo kwa maana ya mkandarasi huyo aanze kazi mara moja kwa kufuata taratibu. Kama kuna mkwamo wowote Ofisi ya Rais- TAMISEMI tutaingilia kati kuhakikisha tunakwamua na kazi inaendelea, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri unaonaje hilo agizo lako lingeenda kwa mameneja wote ambao mradi huo wa TACTIC unaenda?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, napokea na naomba niseme kuwa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri naelekeza kwa Mameneja wote wa TARURA katika mikoa na wilaya ambazo zinatekeleza Mradi wa TACTIC kuhakikisha kuwa wanasimamia kwa karibu hatua zote za manunuzi, lakini pia kuhakikisha kuwa wakandarasi wanafika site kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa miradi hiyo mara moja. Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nulize swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga Soko na Stendi ya Kisongo Mateves ambayo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Saputu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali imeweka utaratibu wa kuhakikisha kwamba, kwanza Halmashauri zenye miradi hiyo zinaainisha gharama zinazohitajika kwa ajili ya ujenzi wa stendi na masoko hayo. Pia, kutenga fedha kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kuanza utekelezaji. Lakini kama gharama ni kubwa kuliko uwezo wa halmashauri, kuwasilisha Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, tutaenda kulitekeleza hilo, na hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais lazima tutaitekeleza na tutaipa kipaumbele katika miradi yetu ya ujenzi wa masoko na stendi.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi; ujenzi wa stendi Mji Mdogo wa Katesh unasuasua; je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kuwa stendi hiyo inakamilika haraka ili ianze kutumika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, natoa maelekezo na nasisitiza kwa Mkurugenzi wa Halmashauri hii ya Hanang. Tulishafanya ziara pale, mimi na Mheshimiwa Mbunge lakini pia tuliona kweli stendi ile inasuasua. Tulitoa maelekezo na Halmashauri ilitoa commitment ya kuongeza fedha kwa ajili ya kukamilisha. Kwa hiyo, tunatoa maelekezo kwamba wahakikishe wanakamilisha stendi ile haraka iwezekanavyo na sisi Ofisi ya Rais-TAMISEMI tutafika kukagua na kuona kazi imetekelezwa kwa wakati, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaanza upya mchakato wa ujenzi wa stendi ya kisasa eneo la Madira, mchakato huo ambao ulisitishwa mwaka 2019 ghafla wakati umefikia hatua ya utekelezaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. John Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nilichukue hili suala la stendi hii ambayo Mheshimiwa Mbunge ameitaja kule Arumeru tuone kwa nini ilisitishwa ghafla mwaka 2019, na hatua zipi zimechukuliwa kuondoa changamoto hiyo ili lengo la Serikali kuwahudumia wananchi kwa kujenga stendi hiyo liweze kukamilika kwa wakati.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona. Swali langu ni katika miji ile 45 na Makambako ipo; je, ni lini Serikali itaanza kujenga stendi na soko kwa Mji wa Makambako?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Mradi wa TACTIC katika Halmashauri ya Mji wa Makambako. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, nafahamu Makambako ipo awamu ya pili au ya tatu. Tunakwenda kusukuma kuhakikisha ujenzi wa stendi na soko katika Mji wa Makambako unaanza mapema iwezekanavyo. Najua taratibu za usanifu zimeshafanyika na zinaendelea kukamilishwa.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa stendi ya mabasi katika Mji wa Babati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, stendi ya mabasi katika Mji wa Babati ni kipaumbele cha Serikali na tulielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Babati na Halmashauri ya Mji wa Babati zianze kuandaa na anafahamu, Halmashauri ya Mji wa Babati iko kwenye mpango wa TACTIC, na mpango huo wa TACTIC unaendelea kutekelezwa kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya msingi kwamba tunakwenda kwa awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu na sasa zinakwenda sambamba kwa kufuatana. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Halmashauri ya Mji wa Babati ipo kwenye TACTIC, lakini kuhusu Halmashauri ya Wilaya ya Babati tutaendelea kuhakikisha kwamba Halmashauri inatenga lakini pia na sisi Serikali Kuu tunaona uwezekano wa ku-support.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mbeya ni Jiji, lakini hauna stendi yenye hadhi ya jiji. Sasa je, ni lini Serikali itajenga stendi Mkoa wa Mbeya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mkoa wa Mbeya ni Jiji na jiji lile kwa bahati nzuri Mbunge wake ni Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson ambaye ni Spika wa Mbunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Serikali inatambua na imeweka kipaumbele kuhakikisha kwamba tunajenga stendi ya kisasa inayoendana na Jiji la Mbeya, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru, Halmashauri ya Wilaya wa Kilwa inaendelea na ujenzi wa Stendi ya Mabasi pale Nangurukuru, lakini uwezeshaji wake wa kimapato ni mdogo. Je, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI, iko tayari sasa kuipa fedha Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa ili ikamilishe ujenzi wa stendi pale Nangurukuru? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ujenzi wa stendi ya mabasi Nangurukuru, ni kweli umeanza kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa. Naomba nitumie fursa hii kusisitiza kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kilwa, kuhakikisha kwamba anaweka kipaumbele kwenye bajeti ya mapato ya ndani kuongeza kasi ya ujenzi wa stendi ile, lakini na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tutafanya tathmini kuona kama wanashindwa, kwa maana ya uwezo wa mapato kukamilisha kwa wakati ili tuone uwezekano wa kupata fedha kwa ajili ya kuwa-support ili kuikamilisha kwa wakati, ahsante. (Makofi)
MHE. SHAMSIA A. MTAMBA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii; je, ni lini sasa Serikali itajenga Stendi na Soko katika Halmashauri yangu ya Wilaya ya Mtwara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ujenzi wa stendi na soko katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara ni moja ya mahitaji ya wananchi na Serikali yetu ya Awamu ya Sita imeweka kipaumbele kusogeza huduma za kijamii kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, sasa nitumie fursa hii pia kuendelea kusisitiza kwamba ni wajibu wa Wakurugenzi wa Halmashauri husika kuweka vipaumbele kupitia mapato ya ndani, kuanza ujenzi wa stendi na soko. Halmashauri zetu nyingi zina uwezo wa kufanya hivyo zikiweka kipaumbele, lakini na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa maana ya Serikali Kuu tutaendelea kufanya tathmini na kuona maeneo ambayo yanahitaji kuongezewa nguvu, tutafanya hivyo ili stendi hizo na masoko yaweze kukamilika kwa wakati, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na Serikali kuendelea kutenga fedha nyingi kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini, bado kuna uhitaji mkubwa wa fedha ambazo ningependa Serikali itenge.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kwenda na mimi akaangalie mazingira ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini ili iwe rahisi kwa Serikali kuendelea kutenga fedha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua kwamba Jimbo la Morogoro Kusini linahitaji fedha zaidi kwa ajili ya utekelezaji wa barabara hizi. Ndiyo maana katika kipindi cha miaka ya fedha mitatu mfululizo, Serikali imeendelea kuongeza bajeti ya barabara katika jimbo hili lakini pia katika majimbo yote.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia kwamba nipo tayari kuambatana naye kwenda katika Jimbo la Morogoro Kusini. Tutakubaliana baada ya maswali haya ili tupange, baada ya Bunge tuweze kwenda na kuona hali ilivyo, lakini pia kushirikiana katika kuboresha huduma hiyo, ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara za Jimbo la Kilwa Kaskazini zilizo nyingi zina hali ya miinuko mikali pamoja na udongo korofi na zina hali mbaya sana. Je, Serikali ina mkakati gani wa barabara za aina hii ili kuboresha na kuhakikisha kwamba zinapitika muda wote wa mwaka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya namna ya kufanya allocation ya fedha za barabara kwenye majimbo. Kwa sababu tunafahamu kwamba hali ya hewa inatofautiana, kuna majimbo yenye mvua nyingi kwa mwaka mzima. Kuna majimbo yenye milima na miteremko mikali, lakini kuna majimbo au wilaya ambazo zina udongo korofi kwa ujenzi wa barabara.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hata ule mgao wa fedha za Bajeti ya TARURA zinakwenda kwa kuzingatia vigezo hivyo, ukiwepo ukubwa lakini na hali ya kijiografia ya maeneo hayo. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge, Serikali inatambua kwamba Kilwa Kusini na Kilwa kwa ujumla ina changamoto hiyo na ndiyo maana inaendelea kuongeza bajeti na tutaendelea kufanya hivyo kuhakikisha kwamba barabara hizi zinapitika vizuri zaidi. Ahsante. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, pamoja na maelezo aliyoyatoa sasa hivi, kulikuwa na ahadi ya Serikali kwamba majimbo yale ya mjini, ambayo yana mjini na vijijini yatapewa bajeti kubwa zaidi upande wa TARURA. Nini kauli ya Serikali kuhusu kutekeleza azma hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli ilikuwa ni ahadi ya Serikali na niseme ahadi hiyo imeanza kutekelezwa. Kwa maana ya Manispaa na miji ambayo ina hali ya miji lakini pia vijijini, Serikali imeendelea kuongeza bajeti kuwezesha barabara za vijijini zijengwe vizuri, pia na barabara za mijini zijengwe vizuri.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge likiwepo Jimbo la Njombe Mjini, tutahakikisha tunaendelea kuboresha utaratibu huu, ahsante. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, napenda kujua ni lini Serikali itajenga daraja la kuunganisha Kata ya Matongo na Kata ya Kibasuka, Nyarwana ili kusaidia mawasiliano wakati wa mvua? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kumwelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Mara, lakini pia Wilaya ya Tarime kwenda kufanya tathmini ya gharama zinazohitajika katika ujenzi wa daraja hili la Matongo linalounganisha upande wa pili, ili sasa Serikali ifanye tathmini kuona kama liko ndani ya uwezo wa bajeti ya kila mwaka au linahitaji special bajeti ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja hilo, ahsante. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Liwale ndiyo wilaya pekee yenye kilometa chache sana za barabara za changarawe na tuna chini ya kilometa nne tu za lami. Je, Serikali haioni umuhimu wa kuiongezea wilaya hii fedha za TARURA ili kuongeza ufanisi wa ujenzi wa barabara hizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli Jimbo la Liwale lina changamoto kubwa ya barabara. Katika bajeti zetu za miaka mitatu mfululizo, Mheshimiwa Kuchauka ni shahidi kwamba bajeti imeendelea kuongezeka, lakini najua bado haitoshelezi kutokana na ukubwa na changamoto kubwa ya barabara.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuboresha suala la kuhakikisha kwamba barabara hizo zinatengewa fedha zaidi ili ziweze kupitika vizuri zaidi, ahsante. (Makofi)
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, Mji wa Iringa ni mji ambao barabara kubwa zote zinapita katikati ya mji; je, ni namna gani Serikali itatusaidia kwa dharura ili kupanua barabara za pembeni kwa kuwaongezea TARURA bajeti?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali lengo lake ni kuhahikisha kwamba barabara zetu zinapitika vizuri zaidi. Pia ni jukumu la halmashauri kuainisha maeneo ambayo wanadhani ni muhimu barabara zipanuliwe vizuri zaidi. Mameneja wa TARURA wa Mkoa na Wilaya wanatakiwa kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kutoa wito kwa Meneja wa TARURA Mkoa wa Iringa, wa Wilaya ya Iringa na Mkurugenzi wa Manispaa ya Iringa, kuainisha barabara hizo, kutambua gharama zinazohitajika ili tuweze kuweka mpango kazi wa utekelezaji kwa awamu, ahsante. (Makofi)
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, Halmashauri ya Wilaya ya Mbongwe imepakana na wilaya nne, lakini bajeti ya TARURA haitoshi na barabara zinahitaji kufunguliwa.

Je, ni lini Serikali Kuu itatoa pesa kwa TARURA ili kusudi njia zinazounganishwa na Wilaya ya Mbongwe ziweze kufunguliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunatambua Wilaya ya Mbongwe inapakana na halmashauri almost nne. Kuna changamoto ya baadhi ya barabara ambazo zinaunganisha Halmashauri ya Mbongwe na halmashauri za jirani. Serikali imeendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaboresha ujenzi wa barabara hizo na tutaendelea kufanya hivyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, kikao cha Mheshimiwa Waziri Mkuu na Mameneja wa TARURA, aliagiza Mikoa ya Kusini hususan Njombe, ikiwemo Wilaya ya Makete kuangaliwa kwa jicho la karibu kutokana na kwamba ni wilaya ambazo mvua zinanyesha kwa muda mrefu na Makete bajeti ya TARURA ni ndogo sana. Je, ni lini Serikali itaongeza fedha hizi na kuzingatia maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli yalikuwa ni maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kazi yetu ni kutekeleza maelekezo hayo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tumeshafanya tathmini ya halmashauri zenye mvua nyingi, milima na aina ya udongo ikiwemo Halmashauri ya Makete na bajeti ya barabara katika Halamashauri ya Wilaya ya Makete itaendelea kuongezwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru na nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa miradi mingi inayotekelezwa na TARURA, kumekuwa na changamoto ya ubora wa wakandarasi wanaotekeleza miradi hii.

Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha katika miradi hii, pamoja na Serikali kutenga pesa nyingi lakini wakandarasi wanaopatikana wawe na ubora wa kuhakikisha barabara zile zinakuwa vizuri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwenye Jimbo la Ukerewe barabara inayounganisha Kata ya Nkilinzya na Kata ya Bukindo kuna daraja pale linaleta shida kubwa sana. Je, ni lini Serikali itatusaidia kupata pesa za kujenga daraja linalounganisha Kata ya Bukindo na Kata ya Nkilizya? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kusisitiza kwa Mameneja wote wa TARURA wa Mikoa na Wilaya, kwamba Serikali ilikwishatoa maelekezo kwamba kila tunapotekeleza miradi ya Barabara, kwanza lazima tupate wakandarasi wenye sifa na uwezo wa kujenga barabara kwa kuzingatia ubora na thamani ya fedha, lakini kukamilisha kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, pili, tulishaelekeza kuchukua hatua kwa wakati kwa wakandarasi ambao wataonesha kutokuwa na uwezo mzuri wa kujenga barabara hizo. Pia, kuhakikisha kwamba ikiwezekana tunavunja mikataba hiyo kwa kufuata taratibu za kisheria na kupata wakandarasi ambao wana sifa hiyo. Kwa hiyo, naomba nisisitize kwenye eneo hili, kwamba ni wajibu wa Mameneja wa Mikoa, pia wa Wilaya lakini na halmashauri zetu na Mabaraza ya Madiwani kuhakikisha kwamba wanajiridhisha na ubora wa barabara kabla mradi haujakamilika.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na daraja linalounganisha Kata ya Bukindo na Nkilizya ambalo liko katika halmashauri ya Ukerewe, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunahitaji kufanya tathmini na hivyo meneja wa TARURA Wilaya afanye tathmini, watuletee gharama. Tutaona kama Serikali Kuu inahitaji kutoa fedha ama mapato ya ndani yanaweza kujenga daraja hilo, ahsante.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Daraja la Makulu Villa ni daraja linalounganisha Wilaya ya Simanjiro na Wilaya ya Same, lakini daraja hili limekuwa na changamoto kubwa kwa kuwa wakulima na wafugaji wanashindwa kufanya biashara zao. Je, Serikali imejipanga vipi katika kujenga daraja hili ili kuwasaidia wananchi hawa? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kuhusu Daraja la Makulu Villa ambalo linaunganisha Halmashauri ya Simanjiro na Same kwamba ni changamoto na linakwamisha shughuli za kiuchumi kwa wananchi, wakulima na wafugaji, naomba Serikali tulichukue hili na tutafanya tathmini kuona uwezekano wa kuweka mpango kwa ajili ya ujenzi au ukarabati wa daraja hilo, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, barabara za milimani zinapowekewa kifusi, mvua inavyonyesha kifusi kinazolewa kwa hiyo Serikali inapoteza fedha nyingi sana. Je, ni lini Serikali itaweka zege katika barabara ya Chome – Tae na Yavumali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba barabara za milimani kwa kweli tukizijenga kwa kifusi mara nyingi baada ya msimu wa mvua barabara zinaharibika kabisa na hivyo thamani ya fedha inapotea na ndiyo maana Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia TARURA tumefanya tathmini ya aina ya barabara kulingana na hali ya kijiografia ya maeneo husika ikiwemo Halmashauri ya Same, ambayo ina milima mingi.

Mheshimiwa Spika, moja ya solution ambayo tumeitafuta, ni kuanza kujenga barabara hizo kwa kutumia mawe. Kwa sababu mara nyingi maeneo yenye miinuko yana mawe pia, lakini pili kutumia zege. Kwa hiyo, kwa hizi barabara ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja, naomba tuzichukue, tufanye tathmini, halafu tuone uwezekano wa kujenga kwa kiwango cha changarawe, ahsante. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante, Mji wa Bunda ni mji unaokua. Serikali iliahidi kujenga barabara za mitaa kwa kiwango cha lami; je, ni lini sasa Serikali itahakikisha inajenga kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, barabara za lami katika Halmashauri ya Mji wa Bunda ni jambo la msingi na Serikali ilishaahidi na imeshaanza utekelezaji kwa awamu. Najua kuna barabara za lami pale zinaunganisha mitaa, lakini nafahamu kwamba kuna uhitaji mkubwa. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili kuhakikisha kwamba tunajenga barabara za lami kwa kadri ya mahitaji ya Mji wa Bunda, ahsante sana. (Makofi)
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi. Mji wa Mtwango, Jimbo la Lupembe ni eneo ambalo linakua kwa kasi sana. Serikali ina mpango gani wa kujenga lami katika eneo la Mtwango na barabara ya kwenda Ikuna? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika naomba kujibu swali la uhitaji wa barabara ya lami katika Mji wa Mtwango ambao unaunganisha Ikuna na Mtwango.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mji wa Mtwango unakua kwa haraka sana lakini tulishaelekeza Meneja wa TARURA kuweka vipaumbele vya ujenzi wa barabara za lami, katika Halmashauri zetu zote katika zile fedha za Bajeti za TARURA tulielekeza kwamba angalau kuwe na kipaumbele cha kuanza ujenzi wa barabara za lami.

Mheshimiwa Spika, naomba nisisitize kwamba Meneja wa TARURA Wilaya ya Njombe asimamie maelekezo hayo, lakini kama fedha ile ya bajeti haitoshelezi afanye tathmini na kuleta Ofisi ya Rais, TAMISEMI tuweze kuona uwezekano wa kupata fedha zingine kwa ajili ya kuongeza nguvu ya utekelezaji wa mradi huo, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, barabara ya kutoka Ilula kwenda Image - Igumu ipo katika mpango wa kujengwa lami kupitia mradi wa RISE. Je, ni lini barabara hiyo itaanza kujengwa ili wananchi wapate barabara bora, kwa sababu barabara hiyo sasa hivi ipo katika hali mbaya sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Mpango wa RISE unaendelea kutekelezwa, ni kweli kwamba barabara hii ya Ilula - Image na Igumu ambayo ameitaja Mheshimiwa Mbunge ziko kwenye mpango huu wa RISE, nimhakikishie kwamba mpango ule unaendelea kutekelezwa na muda utakapofika tutahakikisha kwamba barabara hizo kwa kadri tulivyojipangia mpangokazi, zinatekelezwa kwa kiwango hicho ambacho kimepangwa kwenye mpango wetu. Ahsante sana.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, barabara ya Himo - Sokoni kwenda Lotima ina kilometa 7.5 na Mheshimiwa Waziri Mkuu aliagiza kwamba TARURA waweze kuijenga kwa kiwango cha lami na mmeanza mmejenga mita 800 tu.

Je, mnatoa kauli gani kuhusu kumalizia barabara hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba ni kweli maelekezo ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imekwishaanza kutekeleza kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema, tumeanza na mita 800 lakini tunafahamu barabara ile ina urefu wa kilometa 7.5 tutakwenda kwa awamu, safari ni hatua tumeanza, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutaendelea kuweka kipaumbele kuhakikisha kilometa hizo 7.5 zinajengwa kiwango cha lami, ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza. Kwanza naishukuru Serikali kwa kupeleka fedha zaidi ya shilingi milioni 240 kwenye vituo hivyo vya afya, nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa tuna upungufu wa wahudumu wa afya kwenye vituo vya afya ikiwemo Kafita, Nyijundu, Kalumwa na Nyangh’wale na zahanati zote za Jimbo la Nyang’hwale; je, Serikali iko tayari kutupelekea wahudumu wa afya ili kuweza kukidhi mahitaji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa pamoja na kwamba vituo vya afya vimejengwa vingi lakini bado tuna uhitaji wa ujenzi wa kituo cha afya kwenye Kata ya Busolwa; je, Serikali iko tayari kutujengea kituo cha afya kwenye Kata ya Busolwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Amar kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napokea shukrani zake kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kupeleka fedha nyingi za vifaa tiba katika Jimbo la Nyangh’wale na nchi nzima kwa ujumla. Kuhusu upungufu wa watumishi, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote tumekuwa mashahidi, katika kipindi cha miaka hii miwili Serikali imeajiri watumishi wa kada mbalimbali za afya zaidi ya 17,000 na kuwapeleka katika vituo vyetu vipya pamoja na vya zamani ambavyo vinaendelea kutoa huduma. Kwa hiyo zoezi hili ni endelevu, ajira zitaendelea kutolewa kwa awamu ili kuhakikisha kwamba vituo hivi vinaendelea kupata watumishi wa kutosha na kutoa huduma bora kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali la pili linalohusiana na Kituo cha Afya cha Busolwa, Serikali imeshaweka mkakati wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati katika maeneo ya kimkakati, tukizingatia umbali kutoka kituo cha karibu zaidi, idadi ya wananchi katika maeneo hayo na aina ya jiografia ya eneo husika. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya tathmini kuona Kata ya Busolwa kama inakidhi vigezo, na kama inakidhi vigezo tutaanza na mapato ya ndani ya Halmashauri na baadaye Serikali itaona uwezekano wa kuongeza fedha kwa ajili ya kukamilisha, ahsante sana. (Makofi)
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itamalizia Kituo cha Afya cha Kata ya Kidaru katika Jimbo la Iramba, hasa ukizingatia watu wake wako pembezoni na hivyo hutembea umbali mrefu kufuata huduma hizo za afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali imeanza kujenga kituo cha afya ambacho amekitaja ambacho kipo katika Jimbo la Iramba, na sisi tutahakikisha kituo kile kinakamilika. Ujenzi wa vituo hivi vya afya unakwenda kwa awamu, tuna awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba Serikali itatoa kipaumbele kutafuta fedha ili tukamilishe ujenzi wa kituo hiki cha afya.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Halmashauri ya Mji wa Mafinga imejenga Kituo cha Ifingo na Kituo cha Bumilayinga. Hata hivyo vituo hivi havina huduma kwa ajili ya kulaza akina baba, akina mama na watoto isipokuwa tu kina jengo la mama na mtoto. Je, Serikali iko tayari kutusaidia na kuhakikisha tunapata hizo facilities?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Mafinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iliweka mpango wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati kwa awamu, na katika awamu ya kwanza ilitoa shilingi milioni 500. Kipaumbele ilikuwa ni majengo ya OPD, Maabara, Jengo la Mama na Mtoto pamoja na majengo ya upasuaji na kichomea taka. Hata hivyo, vituo vyote hivi ambavyo vimejengwa bado vinakosa huduma ya wodi ya wanaume, wanawake na wodi ya watoto. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali itaendelea kwa awamu zinazofuata kujenga wodi kwa ajili ya kulaza wanaume, wanawake na watoto ikiwemo katika Kituo hiki cha Ifingo pamoja na Bumilayinga katika jimbo la Mafinga.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza naomba kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa majibu mazuri yanayoonyesha nia na mkakati wa kuanza mradi ule, lakini bado nina swali dogo la nyongeza. Je, Naibu Waziri yuko tayari kutembelea eneo la mradi ili kujionea umuhimu au ukubwa wa uhitaji wa mradi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwanza nipokee pongezi zake kwa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa iliyoifanya katika ujenzi wa vituo vya mabasi nchini kote. Nimhakikishie tu Mheshimiwa kwamba niko tayari baada ya kumaliza shughuli za Bunge, tutakubaliana baada ya kipindi hiki cha maswali na majibu tupange ratiba ya kwenda Tunduru tukapitie pale.

MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itajenga stendi ya mabasi katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nawaelekeza Halmashauri ya Kibondo kufanya tathmini ya gharama zinazohitajika kwa ajili ya ujenzi na kuanza kutenga mapato ya ndani. Lakini kama uwezo hautatosha walete andiko hilo Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya kutafuta fedha za kujengea stendi hiyo.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Momba hatuna stendi hata moja na kuna uhitaji mkubwa; je, ni lini Serikali itatupatia fedha tuweze kujenga kituo cha mabasi ili kitumike kama chanzo cha mapato kwenye Halmashauri yetu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ni wajibu wa Wakurugenzi wa Halmashauri kutambua maeneo kwa ajili ya huduma za kijamii ikiwemo stendi, pia, ni wajibu wao kuanza kutenga fedha kupitia mapato ya ndani na kuwasilisha maandiko Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi huo. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kuwa tunatoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Momba kufanya tathmini ili tujue gharama zinazohitajika ili waanze kutenga mapato ya ndani lakini pia ofisi ya Rais TAMISEMI tuone uwezekano wa kupata fedha kwa ajili ya shughuli hiyo, ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ni kwamba mkopo unaotolewa na NHIF ni wa shilingi milioni 200 na utaifanya hospitali yetu kulipa kiasi cha shilingi milioni 6,500,092 kwa mwezi, katika miezi 36, na itakuwa imelipa jumla ya shilingi milioni 237, pamoja na riba ya asilimia 11.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haioni nia njema ya Wilaya ya Maswa ya kukopa NHIF kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la X–Ray ili Serikali itoe fedha ambayo si mkopo kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo la X–Ray na wananchi wapate huduma?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni lini Serikali vilevile itajenga Kituo cha Afya cha Kata ya Sangamwalugesha katika Kijiji cha Sangamwalugesha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nyongo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya huduma za afya inatumia fedha za Serikali Kuu na fedha zinazotokana na makusanyo ya ndani, zikiwemo fedha za uchangiaji wa huduma za afya lakini pia na za Mfuko wa Bima ya Afya ya Taifa (NHIF).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwapongeze sana Halmashauri ya Maswa na nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge; kwa sababu yeye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii na amekuwa mfano mzuri kuonesha tunaweza tukatumia fursa za mikopo ya NHIF, tukaboresha miundombinu na hatimaye tukatoa huduma bora zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuhakikishie pamoja na kwamba tutakatwa shilingi milioni 6,500,000, bado watakuwa na uwezo wa kuendelea kujiendesha. Pia, jengo litakalojengwa litaongeza mapato ya Hospitali yetu hii ya Maswa.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusiana na hiki kituo cha afya, naomba tulipokee tukafanyie tathmini, tuone kama kinafiti kwenye vituo vya afya vya kimkakati ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya. Ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniruhusu niulize swali la nyongeza.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mahitaji ya jengo la X–Ray katika Wilaya ya Maswa, linafanana kabisa na Kituo cha Afya cha Upuge. Kuna mitambo pale kwa miaka mitano ipo kwenye mabox, X–Ray Mashine na Ultrasound. Lini Serikali itajenga jengo? Kwa sababu mitambo hii itaoza, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchukua fursa hii kwanza kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI; kwamba Serikali ilishapeleka mashine ya X–Ray, ilishapeleka Ultrasound, na wao kupitia mapato ya ndani wana uwezo wa kujenga jengo la X–Ray na Ultrasound ili wananchi waanze kupata huduma hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni wajibu wao, na nitoe wito, kwamba wanatakiwa kuweka kwenye bajeti haraka iwezekanavyo, na ikiwezekana kwenye mapitio ya bajeti mwezi Desemba wananchi waanze kupata huduma za X-Ray na Ultrasound. Ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Iwondo umefikia asilimia 80 lakini fedha za kumalizia asilimia 20 iliyobaki zimekwisha. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa kituo hicho ili wananchi wa kata hiyo waweze kupata huduma?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Kituo cha Afya cha Kata ya Matomondo kimekamilika na sasa kinatoa huduma lakini kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi na hasa kada ya madaktari. Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi katika kituo hicho cha afya ili wananchi wa Kata ya Matomondo waweze kufurahia huduma ya afya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa kwamba Serikali inajenga vituo hivi vya afya kwa awamu. Niwapongeza kwa kujenga kituo cha afya hiki cha Iwondo mpaka kufikia hatua ya asilimia 80 na bado asilimia 20 ya fedha kwa ajili ya ukamilishaji.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kufanya mahesabu tufahamu hii asilimia 20 iliyobaki ni sawa na shilingi ngapi ili tuweze kuona namna ya kupata fedha Serikali Kuu pia na namna ya kupata fedha kutoka kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya kukamailisha ujenzi wa kituo hiki cha afya.

Mheshimiwa Spika, pili, kituo cha afya ambacho kinatoa huduma, Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt, Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka miwili na nusu imeajiri jumla ya watumishi wa sekta ya afya wapatao 17,000 ambao wamepangwa katika vituo mbalimbali kikiwepo kituo hiki. Zoezi hili ni endelevu na tutatoa kipaumbele kwa ajili ya kituo hiki cha afya cha Mpwapwa, ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kata ya Igamba katika Wilaya ya Mbozi ni moja ya kata ambazo zimeahidiwa kupelekewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya. Je, ni lini sasa hizo fedha zitaenda ili ujenzi uanze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kata hii ya Igamba itapelekewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya kama ambavyo Serikali imeahidi, ahsante.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika Kata ya kimkakati ya Kandawale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ujenzi wa vituo vya afya vya kimkakati katika Kata zetu zote nawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali imefanya tathmini na kuainisha maeneo ambayo yana sifa ya kuwa na vituo vya afya vya kimkakati na tutakwenda kujenga vituo hivi vya afya kwa awamu. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge nakuhakikishia kwamba itakapofikika awamu hiyo tutawapatia fedha kwa ajili ya kujenga kituo hicho cha afya, ahsante sana. (Makofi)

MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kuniona. Katika Wilaya ya Chunya zipo Kata chache za kimkakati ambazo hazina vituo vya afya. Je, ni lini Serikali itatenga na kupeleka fedha kwa ajili ya kujenga vituo vya afya kwenye Kata za Luwalaje, Upendo na Kata ya Chokaa katika Kijiji cha Mapogoro? Ahsante.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nampongeza Mheshimiwa Mbunge wa Chunya kwa kuwa na taarifa ya vituo vyake vya kimkakati kama walivyo Waheshimiwa Wabunge wengine. Wameshazileta Ofisi ya Rais, TAMISEMI Serikali inaendelea kutafuta fedha ili ujenzi kwa awamu katika maeneo haya ufanyike. Tutatoa kipaumbele katika Kata ambazo umezitaja, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, Kata za Suji, Vudee na Mshewa ni Kata za kimkakati; je, ni lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kuanza kujenga vituo vya afya hivi vya kimkakati katika maeneo ambayo ameyataja. Nitoe wito na kusisitiza kwamba ni wajibu wa halmashauri kupitia Wakurugenzi na Mabaraza ya Madiwani kuanza kutenga fedha kupitia mapato ya ndani kuanza ujenzi huu na Serikali Kuu itachangia kwa kadri fedha zitakavyokuwa zinapatikana, ahsante. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mmepeleka fedha shilingi milioni 500 na mmechukua milioni 300. Je ni lini inapeleka fedha kwa ajili ya kumaliza kituo cha afya cha Maretadu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa mazingira ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu DC, ambako fedha ya Serikali shilingi milioni 500 ilipelekwa kwa ajili ya kujenga kituo cha afya lakini kwa maamuzi ya Mkurugenzi na Baraza la Madiwani walikiuka utaratibu wakahamisha shilingi milioni 300 kutoka kituo cha afya wakapeleka kwenye mradi mwingine wa hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, naomba kutumia fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Mbulu Vijijini kuhakikisha shilingi milioni 300 waliyoihamisha bila kufuata utaratibu inarejeshwa kwenye kituo cha afya na kukamilisha kituo cha afya kwa haraka iwezekanavyo na sisi ofisi ya Rais, TAMISEMI tutafuatilia, ahsante. (Makofi)
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kubadilisha Zahanati ya Reguruki iiliyoko Jimbo la Arumeru Mashariki kuwa kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Serikali imekuwa na utaratibu wa kupandisha hadhi zahanati ambazo zipo katika maeneo yanayokidhi vigezo vya kuwa vituo vya afya. Kwa hiyo, naomba nipokee hoja ya Mheshimiwa Mbunge kwa zahanati hii ya Reguruki ili tuweze kufanya tathmini na kuona ni kwa kiasi gani anakidhi vigezo vya kuwa kituo cha afya na Serikali ichukue hatua kwa ajili ya kupandisha hadhi, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya Kuuliza swali la nyongeza. Rais wa Awamu ya Tano wakati wa uhai wake alipokuwa katika ziara Wilaya ya Tunduru aliahidi ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Namihungo. Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Rais ya ujenzi wa kituo cha afya katika kituo cha Namihungo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ahadi za Viongozi wetu wakuu wa kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji wa miradi hiyo kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nachukua hoja hii, tayari najua tumeshaanza kuiratibu na tunatafuta fedha na mara fedha zikipatikana tutaleta shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga kituo hiki cha afya, ahsante.

MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa kuwa mimi bado natafuta vituo vitatu vya tarafa, lini Serikali italeta fedha kwa ajili ya vituo vya tarafa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na nakushukuru, naomba tu kumuhakikishia Mheshimiwa Mbunge wa Kiteto kwamba, pamoja na yeye, bado kuna baadhi ya majimbo pia na wilaya zetu ambazo tarafa nzima haina kituo cha afya. Tunafanya mpango wa kuhakikisha kwamba tarafa zote ambazo zina idadi kubwa ya wananchi na kuwa na umbali mrefu kutoka kituo kingine zinapewa kipaumbele kwenye vituo vya afya vya kimkakati. Kwa hiyo nikuhakikishie kwamba tarafa ulizozitaja zitapewa kipaumbele kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Serikali iliahidi kutuma wataalam kwenda kufanya tathmini na uchambuzi ili kijengwe kituo cha afya Kata ya Likawage Jimbo la Kilwa Kusini.

Je, ni lini wataalam hawa watakwenda kufanya tathmini hii ili kituo hicho kijengwe mara moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Suala hili lipo ndani ya uwezo wa wataalam wa Mkoa wa Lindi. Tuna Mganga Mkuu wa Mkoa wa Lindi na tuna Mganga Mkuu wa Wilaya ya Kilwa. Natoa maelekezo, ndani ya siku 14 wawe wamefanya tathmini ya vigezo kama tunahitaji kujenga kituo cha afya hapo lakini wawasilishe Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tufanye maamuzi kwa ajili ya kuanza kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi. Nashukuru.

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa kata ya Ikuna ni miongoni mwa kata za kimkakati na ni kata ambayo ina wakazi wengi, na wananchi wameshaanza kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao zaidi ya miaka miwili.

Je, ni lini Serikali itatupatia kiwango cha fedha ili tumalizie kituo hicho cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nawapongeza wananchi wa Kata hii ya Ikuna kwa kuanza kujenga kituo cha afya kwa nguvu zao. Tutakwenda kuchangia nguvu za wananchi kumalizia kituo hichi cha afya baada ya kufanya tathmini ya kuona hatua waliyofika na kiasi gani cha fedha kinahitajika. Lakini pia nimuombe Mkurugenzi wa Halmashauri atenge fedha pia za mapato ya ndani wakati tunatafuta fedha za Serikali Kuu. Ahsante.

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, je, ni lini Serikali itajenga upya ama kukarabati jengo la wagonjwa wa nje (OPD) katika Kituo cha Afya Likombe kilichopo Manispaa ya Mtwara Mikindani? Jengo hilo limechakaa, na la zamani, halikidhi mahitaji ya sasa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kutumia fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara Mikindani, kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI tathmini ya gharama zinazohitajika kwenye kufanya ukarabati lakini pia kama ni kufanya ujenzi mpya, ili tuweze kuona kama gharama hiyo ipo ndani ya uwezo wa mapato ya ndani ya Halmashauri. Tutatoa maelekezo ili waanze kutenga fedha mwaka wa fedha 2024/2025. Kama ipo nje ya uwezo wao, Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa maana ya Serikali Kuu, itaangalia namna ya kuwaunga mkono kupitia fedha ya Serikali Kuu.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa kodi inayokatwa katika matumizi ya mfuko huu ni kubwa sana, ni lini Serikali itaenda kuondoa kodi hiyo katika matumizi ya Mfuko wa Jimbo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa Wakurugenzi wetu wengi ni wapya ambao wamechaguliwa katika kuendesha halmashauri zetu. Je, ni lini Serikali itakwenda kupeleka mafunzo kuwawezesha Wakurugenzi hawa kujua thamani ya Mfuko wa Jimbo kwa Waheshimiwa Wabunge? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, naomba tulipokee suala la kodi inayokatwa katika fedha za Mfuko wa Jimbo na hususan kwa upande wa Zanzibar. Suala hili ni la kiutaratibu, tutafanya utaratibu kuhusiana na Wizara ya Fedha lakini pia Wizara ya Muungano, Ofisi ya Rais TAMISEMI, kwa pamoja tuweze kuona njia nzuri zaidi ya kurekebisha changamoto hii ili tuweze kwenda vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili kuhusiana na Wakurugenzi wengi kuwa wapya. Ni kweli na tunahitaji kuona Wakurugenzi wetu wanaelewa vizuri wajibu wao wa kutekeleza Mfuko wa Jimbo. Nitumie fursa hii kwanza, kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya mafunzo kwa Wakurugenzi wote ili wajue wajibu wao katika kusimamia Mfuko wa Jimbo.

Mheshimiwa Spika, natoa msisitizo kwa Wakurugenzi wote kote nchini, kumekuwa na changamoto, Waheshimiwa Wabunge wanakaa na Kamati za Mfuko wa Jimbo, wanapitisha miradi lakini Wakurugenzi wanazuia fedha zisiende kutekeleza miradi ile.

Mheshimiwa Spika, naomba kutumia fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, kuelekeza kwamba Mkurugenzi yeyote atakayekiuka utaratibu baada ya Mwenyekiti wa mfuko huo kuidhinisha matumizi, tutachukua hatua kali za kinidhamu dhidi yake. Miradi hii itekelezwe kwa wakati baada ya Waheshimiwa Wabunge kupitisha miradi hiyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa fedha za Mfuko wa Jimbo zinategemea sana idadi ya watu kwenye majimbo yetu, na ni ukweli sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 imekamilika na hivyo tunazo takwimu mpya kwenye majimbo yetu.

Je, katika mwaka wa fedha 2023/2024 fedha zitakazotolewa zitazingatia idadi ya watu kwenye majimbo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba fedha za Mfuko wa Jimbo zinategemea idadi ya wananchi katika jimbo husika, ukubwa wa kijiografia lakini pia na kasi ya umaskini katika eneo husika.

Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kwanza Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kipindi cha mwaka wa fedha uliopita iliongeza fedha za Mfuko wa Jimbo. Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi; iliongezeka na imeendelea kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa miradi hiyo. Suala la kuzingatia matokeo ya sensa ya mwaka jana ni muhimu na Serikali itaendelea kufanya kazi kwa sababu moja ya kigezo ni idadi ya watu katika maeneo hayo. (Makofi)
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, hata hivyo, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, imekuwa ni kawaida ya Serikali kuwapangia watumishi Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa na kuwahamisha kabla hawajaripoti hasa madaktari, je, nini mpango wa Serikali kutoa ajira mbadala kwa nafasi hizo ambazo madaktari hawakuripoti?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kumekuwa na changamoto ya wananchi kulazimika kuajiri walinzi kwa ajili ya kulinda shule za sekondari na zahanati, je, nini mkakati wa Serikali kuajiri walinzi hawa ili waweze kulipwa na mafao yao ya uzeeni? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kwanza, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Kamonga, kwamba kwa utaratibu wa ajira ulioanza mwaka wa fedha 2021/2022. Kwanza ajira zinaombwa kwa njia ya mtandao kwa maana kwa njia ya kielektroniki. Kuna mfumo mahususi wa ajira lakini wanaoomba ajira wanaomba kituo mahsusi kwa maana ya ndani ya halmashauri husika na kituo husika.

Mheshimiwa Spika, tumeshaweka utaratibu kwamba, lazima waripoti na hawawezi kuhamishwa ndani ya miaka mitatu ya kwanza katika maeneo yao. Naomba kuchukua suala hili la Ludewa, tulifanyie ufuatiliaji kama kuna madaktari walipangiwa na kabla hawajaripoti walihamishwa, tuone ni kwa sababu gani hatua hizo zilichukuliwa kinyume na taratibu za ajira ambazo zimewekwa kwenye mfumo wa ajira kukaa angalau miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kuhakikisha kwamba halmashauri zote za pembezoni, zinapangiwa watumishi zaidi kuliko za mijini kwa sababu za pembezoni zina upungufu mkubwa. Tutahakikisha kwamba hatuhamishi bila sababu za msingi kwa watumishi kutoka halmashauri za pembezoni.

Mheshimiwa Spika, kuhusu wananchi kuajiri walinzi katika shule na maeneo mengine kama zahanati. Tulielekeza kwamba Serikali za Vijiji ziweke utaratibu rafiki kwa wananchi kuona uwezekano wa kulinda rasilimali za shule. Lakini zahanati na vituo vingine vya huduma bila kuwaumiza wale walinzi kwa maana kuwalipa posho zao na kuhakikisha kwamba wanawekewa fedha kwa ajili ya kiinua mgongo pale wanapostaafu kwa taratibu zile za ajira za mikataba, ahsante. (Makofi)

MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipatia fursa hii. Jimbo la Newala Vijijini lina jumla ya walimu 475 kati ya walimu 787 wanaohitajika kuwepo.

Je, ni lini Serikali itapeleka walimu 312 ambao ni upungufu katika Jimbo la Newala Vijijini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuajiri watumishi wa Kada ya Elimu na pia imeendelea kupeleka walimu katika Halmashairi ya Newala Vijijini lakini tunatambua kwamba bado kuna upungufu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba kadri Serikali itakavyokuwa inaajiri walimu, tutatoa kipaumbele katika Halmashauri ya Newala Vijijini. Ahsante.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Halmashauri ya Mji wa Nanyamba ina upungufu wa watumishi wa Sekta ya Afya takribani asilimia 60 ya mahitaji yake.

Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha katika Halmashauri ya Mji wa Nanyamba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha miaka miwili ya Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kazi kubwa sana ya kuajiri wataalam wa afya imefanyika. Jumla ya watumishi wa kada mbalimbali za afya wapatao 17,000 wameajiriwa na kupelekwa katika halmashauri zote kote nchini ikiwepo Halmashauri ya Mji wa Nanyamba.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu bado kuna upungufu, namuhakikishia Mheshimiwa Mbunge, kwamba kadri tutakavyoendelea na ajira nyingine za wataalam wa afya, tutatoa kipaumbele kwa Halmashauri ya Mji wa Nanyamba. ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi. Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ina upungufu wa watumishi wa kada ya ualimu wapatao 1000 na kada ya afya wapatao zaidi ya 200.

Je, ni lini Serikali itaenda kutatua kero ya watumishi kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, utatuzi wa changamoto ya upungufu wa wataalam wa sekta ya elimu na afya ni mchakato, safari ni hatua, tumeanza. Katika Halmashauri ya Tanganyika nafahamu ni moja ya halmashauri ambazo zilipata watumishi wengi sana katika ajira mbili zilizopita ukilinganisha na halmashauri nyingine kwa sababu ya vigezo vya kuwa ipo mbali zaidi lakini ilikuwa na upungufu mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kwamba zoezi ambalo limeanza la kupeleka watumishi kwa wingi Tanganyika, litaendelea kadri tutakavyokuwa tunaendelea kuajiri watumishi wa sekta hizo. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuweza kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa kuna upungufu mkubwa wa walimu katika shule za msingi na sekondari Mkoa wa Simiyu hasa walimu wa sayansi; je, ni lini Serikali itapeleka walimu wa kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Simiyu ni miongoni mwa mikoa 11 ambayo Ofisi ya Rais - TAMISEMI iliiainisha ikiwa ni mikoa yenye upungufu mkubwa zaidi wa watumishi wa sekta ya elimu, lakini pia wa sekta ya afya. Kila ajira zinapotokea, mikoa hii inapewa kipaumbele cha hali ya juu zaidi kuliko mikoa mingine ambayo ina nafuu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ajira mbili zilizopita walivyopata watumishi wengi Mkoa wa Simiyu, tutaendelea kupeleka watumishi wengi ili waweze kupunguza pengo la watumishi katika vituo lakini na shule zetu, ahsante.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina mwaka wa nane hapa Bungeni, sijawahi kuona mjadala wowote wa kupandisha posho za Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji. Napenda Mheshimiwa Waziri atueleze, ni lini mara ya mwisho Serikali ilipitia…

SPIKA: Mheshimiwa, hujawahi kuona nini? Samahani.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, sijawahi kuona mpango wa Serikali kupandisha posho za viongozi hawa. Napenda kujua, ni lini mara ya mwisho Serikali ilipitia posho za Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; Serikali kwa kuwa Mheshimiwa Rais Dkt. Mama Samia amepeleka fedha nyingi sana vijijini na zinahitaji umakini wa usimamizi ili miradi iweze kukamilishwa kiukamilifu.

Je, kwa mwaka wa fedha ujao 2024/2025 Serikali ipo tayari kuongeza posho ya Madiwani, Wenyeviti wa Vijiji na Mitaa ili kupunguza kelele za viongozi hawa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwanza namuhakikishia Mheshimiwa Mbunge, kwamba katika Bunge la Bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023, Ofisi ya Rais - TAMISEMI katika mjadala ambao Waheshimiwa Wabunge waliujadili kwa kina sana, ilikuwa ni uwezekano wa kuongeza posho za Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti, na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, Bunge hili limeshajadili sana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI tulipokea, nimhakikishie kwamb lini posho hizi zilipandishwa, posho za Waheshimiwa Madiwani zilipandishwa. Nitakwenda kuona exactly ni lini lakini nafahamu kwamba zilipandishwa kutoka zilipokuwa, kidogo lakini sasa angalau ziko na hali nzuri.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba zinahitajika kuongezeka zaidi ili ziweze kukidhi mahitaji na safari ni hatua. Serikali inaendelea kulitazama na kuona uwezekano huo wa kupandisha posho za Waheshimiwa Madiwani.

Mheshimiwa Spika, pili, katika mwaka ujao wa fedha, kama tutaongeza posho hizo au vinginevyo. Tumelichukua, Serikali itafanya tathmini na kuona uwezekano huo na itatoa taarifa rasmi kama linawezekana ama tunahitaji kuijengea uwezo ili kuweza kuongeza posho hizo, ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa uzoefu ambao nimeupata kujifunza kwenye halmashauri mbalimbali nchini, kumekuwa na halmashauri nyingi ambazo zinavuka na bakaa kwa maana ya salio.

Je, Serikali haioni ni wakati sahihi kuzielekeza halmashauri zote nchini kutumia mapato ya ndani kuwaongeza Madiwani kwa sababu sehemu kubwa Serikali imechukua mzigo huo na halmashauri nyingi zimekuwa zikivuka na bakaa na salio?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ni kweli kuna baadhi ya halmashauri zimekuwa zikivuka na fedha katika mwaka wa fedha unapoisha kwenda mwaka mwingine kwa maana ya bakaa na Mheshimiwa Mbunge anapendekeza kwamba salio lile litumike kwa ajili ya kuwalipa nyongeza posho Waheshimiwa Madiwani, lakini niseme zile fedha ambazo zinavuka mwisho wa mwaka wa fedha mara nyingi ni fedha za miradi ambayo inasubiri kutekelezwa. Kwa hiyo, ni fedha ambazo tayari ziko committed, lakini zinakwenda kutekeleza miradi ile katika first quarter ya mwaka wa fedha unaofuata.

Mheshimiwa Spika, jambo la msingi ni kwamba tunajua kuna umuhimu wa kuongeza posho Waheshimiwa Madiwani, Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ni jambo ambalo tutaendelea kulifanyia kazi na kadri uwezo wa Serikali utakapoongezeka suala hilo litaendelea kushughulikiwa, ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante, ningependa kufahamu je, Serikali ipo tayari kupitia upya posho kwa ajili ya vikao vya Madiwani kwa kuzingatia umbali wanakotoka kwa sababu kama Wilayani Muleba tunazo Kata tano Boziba, Kerebe, Rubale, Ikuza na Mazinga ambazo ni za visiwani lakini Waheshimiwa Madiwani wakienda kwenye vikao wanalipwa posho sawa na wale ambao wanatoka pale pale mjini wakati wao wakienda kwenye vikao inawalazimu walale kutokana na umbali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwishatoa mwongozo wa posho za kujikimu kwa Waheshimiwa Madiwani wanapohuduhuria vikao vya mabaraza na mwongozo ule ulizingatia wale ambao wanatoka mbali wanahitaji kulala, rate zao zilikuwa ziko tofauti na wale ambao wanatoka eneo la jirani hawahitaji kulala rate zao ziko tofauti.

Kwa hiyo, nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuwasisitiza Wakurugenzi wa Mamlaka za Halmashauri zote kuzingatia mwongozo ambao uko very clear na unaelekeza wanaotoka mbali wanatakiwa kulipwa kiasi gani na wale wanaotoka jirani wanatakiwa kulipwa kiasi gani, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona, kwa kuwa Serikali imeondoa mzigo ule wa kulipa posho za Madiwani kutoka kwenye Halmashauri na Serikali Kuu sasa ndio inayolipa hizo posho; je, Ofisi ya Rais, TAMISEMI iko tayari sasa kuelekeza kwamba zile posho zilizokuwa zinalipwa kwa Madiwani sasa zielekezwe kuwalipa Wenyeviti wa Serikali za Vijiji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kutambua kazi kubwa inayofanywa na Waheshimiwa Madiwani kuanzia mwaka wa fedha 2022/2023 alichukua jukumu la Serikali Kuu kulipa posho za Halmashauri 168 kote nchini na kazi hii inaendelea.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba halmashauri hizi siku za nyuma zilikuwa zinalipa posho za Madiwani, lakini zile fedha zimeendelea pia kupelekwa kwenye maeneo ya miradi mbalimbali. Naomba tuchukue wazo la Mheshimiwa Mbunge kwamba tuone kama zinaweza zikapelekwa kwenye malipo ya Serikali za Vijiji na Mitaa, tutafanya tathmini tuone kama inaweza kutekelezwa ama vinginevyo na tutaleta taarifa rasmi, ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na ukiukwaji wa kikanuni na hasa kuhusiana na suala zima la ziara ya Kamati za Kudumu za Madiwani na kwamba kila robo ya mwaka Kamati za Kudumu zinatakiwa kutembelea na kuona miradi iliyotekelezwa katika kipindi hicho, ili kuona kwamba fedha zinazotumwa na Serikali chini ya Mama Samia Suluhu Hassan zinasimamiwa na kuona ile value for money. Sasa Finance Committee peke yake imekuwa ikienda kwenye ziara hii kinyume na kanuni na Kamati nyingine za kudumu zisiende…

SPIKA: Swali lako.

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nini tamko la Serikali kuhusiana na changamoto hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ziara za Kamati za Kudumu za Waheshimiwa Madiwani katika Baraza la Madiwani zimewekwa kwa mujibu wa mwongozo ambao umeelekeza Kamati ya Fedha kutembelea miradi, lakini pia Kamati za Kudumu nyingine kama Huduma za Elimu, Afya na Maji na nyingine kutembelea miradi pia kuona utekelezaji wa miradi ile.

Kwa hiyo, nitumie fursa hii pia kuwasisitiza Wakurugenzi na Mabaraza kuzingatia Mwongozo wa Serikali ambao umetolewa ili kuweza kuwa na ufatiliaji wa karibu wa thamani ya fedha katika miradi ambayo inatekelezwa, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hospitali ya Wilaya ya Makete ni moja kati ya hospitali chakavu sana. Ni hospitali ambayo imetembelewa na Mawaziri tofauti, Mheshimiwa Ummy akiwa TAMISEMI amefika, Mheshimiwa Bashungwa, Mheshimiwa Jafo amefika na Kamati ya Bunge ya TAMISEMI imefika wamejionea hali ya Hospitali ya Wilaya ya Makete.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ipi ni kauli ya Serikali mimi kama Mbunge ningeomba msifanye ukarabati mjenge. Je, ipi ni kauli ya Serikali?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, tuna vituo vya afya cha Kitulo, tunayo zahanati ya Nungu, Kisungilo na Unyangogo, hizi zahanati zimekamilika hazina vifaatiba. Je, ni lini Serikali itapeleka vifaatiba ili huduma zianze kutolewa kwa sababu wananchi wangu wa Makete, wametoa nguvu kazi yao wamejenga zahanati hizi na vituo vya afya lakini vifaatiba hamna. Ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Sanga kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa wananchi wa Jimbo la Makete, nimhakikishie kwamba Serikali itaendelea kumpa ushirikiano ili kuhakikisha wananchi wa Makete wanapata maendeleo ambayo yanatarajiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Makete ni kweli ni hospitali chakavu, Mheshimiwa Mbunge ameuliza hapa mara kadhaa Serikali hii sikivu ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ikamuahidi kupeleka fedha na sasa tumetenga mwaka ujao wa fedha milioni 900. Hii ni miongoni mwa hospitali 19 ambazo mwaka ujao wa fedha zitakabarabitiwa au kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kauli ya Serikali ni kwamba tunafanya tathmini na kuona hospitali zile zenye uchakavu mkubwa beyond repair tunafanya ujenzi mpya, lakini zile ambazo zinaweza kukarabatika, tutakarabati. Kwa hiyo, kauli ya Serikali ni kwamba kufuatia tathmini ambayo tutaifanya katika hospitali ya Makete tutatoa maelekezo rasmi kwamba Shilingi Milioni 900 inakwenda kujenga ama inakwenda kukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Vituo vya Afya vya Kitulo, Zahanati ya Nungu na nyingine kuhitaji vifaatiba. Katika mwaka wa fedha ujao, Serikali imetenga milioni 450,000 kwa ajili ya vituo vya afya na zahanati katika Jimbo la Makete ili vituo hivi viweze kupata vifaatiba. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Naibu Waziri, wananchi wa Kata ya Gale, na Kata ya Makanya, wamejenga viuo vya afya kwa nguvu zao wenyewe.

Je, ni lini Serikali itatoa milioni 250 kama ilivyokuwa inatoa fedha hizo kwenye vituo vingine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeweka mkakati ambao umeendelea kutekelezwa na Waheshimiwa Wabunge wote ni mashahidi kwamba Serikali imeendelea kupeleka fedha Milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya, tumeendelea kupeleka Milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati na hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi vituo ambavyo wananchi wameanza ujenzi, Serikali itapeleka fedha ili tuweze kukamilisha ujenzi huo, ahsante. (Makofi)
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi tena. Nishukuru majibu ya Serikali yaliyotolewa kwa swali, lakini niombe kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza jumla ya barabara ambazo zilijengwa 2021/2022 na zitakazojengwa mwaka wa kesho zinaonesha wastani wa kilomita 100 tu kwa mwaka. Sasa basi jumla ya barabara zinazohudumiwa na TARURA ni zaidi ya kilomita 900, hii maana yake ni kwamba itatuchukua zaidi ya miaka tisa kujenga barabara zote zilizo chini ya TARURA katika Jimbo la Serengeti. Sasa basi Serikali haioni haja ya kutafuta fedha za ziada kwa ajili ya kuongezea Jimbo la Serengeti kwa sababu barabara ni nyingi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; tarehe 25 Julai, 2021, Naibu Waziri wa TAMISEMI aliwaahidi wananchi wa Serengeti kwamba barabara ya lami inayozunguka soko la Mugumu ingejengwa na kukamilishwa. Mpaka sasa hivi mkandarasi ameshasaini mkataba toka mwanzo wa mwaka huu lakini barabara ile haijengwi. Tunaomba commitment ya Serikali ya kujenga barabara ile ya lami ya kuzunguka soko la Mgumu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Msabi kwa kazi nzuri anayoifanya kwa kuwakilisha ipasavyo wananchi wa Jimbo la Serengeti. Pili, kuhusiana na fedha ambazo zinatengwa kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika Halmashauri ya Serengeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hii imeendelea kuongeza fedha ambazo zinakwenda kufanya matengenezo na ujenzi wa barabara vijijini na mijini. Kwa mfano, katika mwaka wa fedha 2020/2021, bajeti ya Serikali kupitia TARURA ilikuwa bilioni 255, lakini 2021/22 Serikali iliongeza kutoka 255 mpaka bilioni 722, zaidi ya mara tatu ya bajeti. Pia mwaka ujao wa fedha tumeongeza kutoka 722 mpaka bilioni 822 plus.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii yenyewe inaonyesha namna Serikali ambavyo ina commitment kubwa ya kuongeza fedha kupitia TARURA ili barabara zetu ziendelee kujengwa. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hata wao mwaka 2020/2021, bajeti ilikuwa ndogo, lakini imeendelea kuongezeka na tutaendelea kuhakikisha tunaongeza bajeti ili barabara za Serengeti zijengwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na barabara ya lami inayozunguka Soko la Mugumu, naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi na Watendaji wote wa Mamlaka hii ya Barabara TARURA kuhakikisha mkandarasi huyu anaanza kazi haraka iwezekanavyo na vinginevyo tutachukua hatua mapema iwezekanavyo ili kuhakikisha barabara inakamilika mapema. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kata ya Lahoda ndio kata maarufu sana kwa uzalishaji wa ufuta na alizeti kwa Kanda ya Mashariki, lakini barabara yao ya kutoka Ilasee, Lahoda hadi Handa na kuunganisha na Singida ni mbovu sana. Naomba kujua nini mkakati wa Serikali wa kuboresha barabara hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana kwa kazi nzuri anayoifanya kwa Jimbo la Chemba na nimhakikishie kwamba Serikali imeweka mkakati mzuri sana kuhakikisha maeneo yote yenye mazao ya kimkakati kama alizeti, ufuta na kata ambazo amezitaja, kutenga bajeti kwa ajili ya kuhakikisha kwamba barabara zile zinajengwa vizuri zinapitika vizuri ili wananchi waweze kusafirisha vizuri mazao yao. Kwa hiyo nitoe maelekezo kwa Meneja wa TARURA Chemba, wafanye tathmini ya bajeti iliyopo na kuweka kipaumbele kwenye maeneo yenye uzalishaji mkubwa kama haya ili barabara ziweze kupitika vizuri. Ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa hii ya swali la nyongeza. Barabara ya Chombe, Kaoze ni barabara muhimu sana na mvua za mwaka jana zilipelekea uharibifu mkubwa na ombi maalum lipo tayari Wizarani. Nataka kujua je, ni lini Serikali itaijenga barabara hii ya Chombe, Kaoze ambayo ni muhimu kwa uchumi wa Kata ya Kaoze?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sangu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kufuatia mvua barabara zetu nyingi zimeathirika na Serikali imefanya tathmini, lakini wataalam wote Mameneja wa Mikoa na Halmashauri wameelekezwa kuleta maandiko maalum ya mapendekezo, lakini na gharama ya utengenezaji wa barabara hizo. Niwapongeze halmashauri hii wameshaleta andiko hilo, tunalifanyia kazi na mapema iwezekanavyo tutaona uwezekano wa kwenda kufanya matengenezo ili barabara ipitike vizuri. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize swali la nyongeza. Changamoto za barabara Arumeru Mashariki zinasababishwa na hali ya kijiografia ambayo sio rafiki wananchi wengi wako milimani. Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kutenga fedha za kutosha kwa ajili ya matengenezo ya barabara hizi kwa kiwango cha lami au kwa teknolojia nyingine yoyote ambayo itafanya barabara hizi zihimili mafuriko wakati wa mvua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Pallangyo kwa kazi kubwa na nzuri anayoifanya kwa Jimbo la Arumeru Mashariki. Pia nimhakikishie kwamba tunafahamu na tumefanya tathmini ya barabara ambazo ziko milimani katika Jimbo la Arumeru Mashariki na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kupitia TARURA tumeweka mpango kazi wa kutenga fedha kulingana na uhitaji. Kuna maeneo yenye milima yenye mvua nyingi na changamoto kadhaa. Kwa hiyo bajeti zetu sasa pamoja na vigezo vingine itazingatia sana hali ya hewa, lakini pia na uhitaji mkubwa wa barabara hizo. Kwa hiyo nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hili tunalifanyia kazi.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza kabisa kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Singida Vijijini, inakabiliwa na ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa. Je, ni lini Serikali itapeleka gari katika hospitali hii ili kuokoa vifo vya kinamama wajawazito na watoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kituo cha afya cha Sepuka, kiko pembezoni na hakina gari la kubebea wagonjwa. Je, ni lini Serikali itapeleka gari katika kituo hiki cha afya?

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kwali kwamba ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Singida Vijijini inahitaji gari la wagonjwa na Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wananchi wote katika Halmashauri zetu kote nchini itapeleka magari ya wagonjwa ndani ya mwaka huu wa fedha au mapema mwaka ujao wa fedha ikiwemo Halmashauri ya hii ya Singida Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Sepuka ambacho kiko pembezoni, tumefanya tathmini ya kuona vituo ambavyo viko pembezoni ambavyo vinahitaji magari ya wagonjwa vitapelekewa magari ya wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, amekuwa akifuatilia sana masuala ya maendeleo ya wananchi wa Mkoa wa Singida na Watanzania kwa ujumla nimhakikishie kwamba tutaendelea kumpa ushirikiano. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nataka nimuulize swali Naibu Waziri, kuna Halmashauri zingine zina Majimbo zaidi ya mawili au matatu, sasa kama mtapeleka gari moja, hilo gari litaenda kwenye Jimbo gani? Kwa nini usiweke wazi, kwa nini isiwe kwa Majimbo badala ya kuwa Halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mpango wa kupeleka magari ya wagonjwa kwenye Halmashauri unazingatia vigezo, kigezo cha kwanza ni idadi ni ya watu katika Halmashauri, kigezo cha pili ni idadi ya wagonjwa kwa maana ya burden of disease katika Halmashauri husika. Utaratibu huu hauzingatii Majimbo kwa sababu Majimbo pia yanatofautiana na idadi ya wananchi ukilinganisha na Halmashauri. Kwa hiyo, tutakwenda kupeleka magari haya, kwa kigezo cha Halmashauri na idadi ya watu na burden of disease. Pale ambapo itahitajika kwa Majimbo mawili kupata gari tutafanya hivyo. (Makofi)
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kufahamu ni lini Serikali itatujengea Kituo cha Afya, katika Kata ya Bara ili kupunguza idadi ya vifo vya mama na mtoto katika Wilaya ya Mbozi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeandaa mkakati, kwanza wa kukamilisha vituo vyote zahanati na hospitali za Halmashauri ambazo zimekamilika lakini hazijaanza kutoa huduma. Baada ya hapo tutakwenda sasa kujenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati likiwemo eneo hili ambalo Mheshimiwa Juliana Shonza amelisema.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutakwenda kuhakikisha kwamba tunajenga pia kituo cha afya baada ya kukamilisha vituo vingine.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na hivyo naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa wananchi wa Ludewa wamevuja jasho sana kuanza ujenzi kwenye Kata 12, Je, ni lini Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuambatana na mimi ili kwenda kushuhudia jinsi wananchi walivyojitoa kutoa kujenga vituo vya afya na havijamaliziwa na Serikali?

Swali la pili, kwa kuwa Tarafa ya Mwambao haina usafiri wa magari na meli kwa muda mrefu haipo. Je, ni kwanini Serikali isitafute boti moja ya mwendokasi ambayo itasaidia wagonjwa kuanzia Lumbila, Kilondo, Makonde, Lifuma, Mkali mpaka Manda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kamonga, amekuwa akifuatilia sana miradi ya maendeleo kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Ludewa, ikiwemo vituo vya afya na magari ya magonjwa. Kwa kweli katika Kata hizi 12 ambazo wananchi wamechangia nguvu zao kujenga vituo vya afya, nimhakikishie kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuunga mkono juhudi za wananchi kukamilisha vituo hivi.

Mheshimiwa Spika, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa, kwa mwaka ujao wa fedha baada ya mwaka huu ambao tumeshaupangia bajeti atenge fedha kwa ajili ya kujenga maabara na kichomea taka kwenye vituo ambavyo wananchi wameshaweka nguvu zao, ili huduma za OPD zianze na Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ambulance, boti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafanya tathmini maeneo yote ambayo ni magumu kufikika ya visiwa na ambayo yanapitiwa na mikondo ya maji, tuangalie uwezekano wa kupata ambulance hizi za boti kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na tutatoa kipaumbele kwenye Wilaya ya Ludewa.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya katika Kata ya Miula Jimbo la Nkasi Kusini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaweka mkakati wa kuainisha maeneo ya kujenga vituo vya afya, ikiwemo katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, kwa hivyo, kadri ya upatikanaji wa fedha katika bajeti inayofuata tutahakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 kuna Kata ya Tumbi pamoja na Kata ya Misha tayari vituo vya afya vimeashaanza kujengwa na vipo katika hali ile ya kumalizia. Ni lini Serikali italeta fedha hizi za kumalizia vituo hivyo vya afya viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kata nyingi bado zinahitaji vituo vya afya, lakini Kata za mkakati tumekwishaziainisha na Waheshimiwa Wabunge, walileta Kata za kipaumbele tatu kila Jimbo, niwahakikishie kwamba Serikali inaendelea kuandaa bajeti kwa ajili ya kuendelea na ukamilishaji wa vituo hivi vya afya, vikiwemo hivi vituo vya afya viwili ambavyo vipo katika Jimbo la Tabora Mjini.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali ndiyo ilihamasisha ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo mbalimbali nchi nzima na kuwahamasisha wananchi washiriki lakini leo hazijakamilisha. Je, mliamua kuwahamasisha wananchi bila kuwa na fedha za kutosha ndiyo maana kila Mbunge leo anaulizia kituo cha afya. Kwa nini sasa msikamilishe wakati ninyi ndiyo mliwahamasisha wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tukubaliane kwamba kuhamasisha wananchi kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa vituo vya afya ni dhamira njema na jambo jema kwa sababu wananchi wetu wamekuwa wanasafiri umbali mrefu sana kupata huduma za afya. Kwa hiyo, kwa kuanza tu jambo hilo lilikuwa ni jema na nia njema ya Serikali lakini tumeendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma.

Mheshimiwa Spika, mwaka uliopita maboma 555 ya zahanati Bilioni 33.5 zilipelekwa, mwaka huu tumepeleka katika maboma zaidi ya 234 ya vituo vya afya na zahanati. Mwaka ujao tunayo maboma 300 ya zahanati ambayo yanakwenda kukamilishwa. Kwa hiyo, Serikali inafanya kazi ya kukamilisha maboma hayo kwa nia njema ya kusogeza huduma kwa wananchi, lakini safari ni hatua, tutakwenda kwa awamu mpaka kukamilisha majengo hayo yote. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Lazaro Londo, inaonekana fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya barabara hiyo haitoshi. Sasa ni nini comment ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hiyo inatengewa fedha za kutosha ili iweze kujengwa na kukamilika na wananchi waitumie?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara hii ya Kisanga, Malolo na Uleling’ombe ni barabara ambayo inatumika kama barabara mbadala kipindi barabara ya kwenda Iringa ya lami inapokuwa ina hitilafu. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa na inatumika kipindi chote cha mwaka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. NDUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo yaliyoulizwa na Mheshimiwa Florent Kyombo kwa niaba yake, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii lakini fedha haitoshi. Kimsingi tunafahamu kwamba safari ni hatua, tunaanza na hatua moja tunakwenda na hatua nyingine, angalau Serikali imeanza kuweka fedha, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kutafuta fedha kukamilisha barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hii barabara nyingine ambayo inaunganisha maeneo haya muhimu ya Kata hizi mbili ya Kisanga na Uleling’ombe nayo iko kwenye mpango. Nimeeleza hapa na tutahakikisha kwamba tunaendelea kutafuta fedha kujenga barabara hizi kadri ya upatikanaji huo. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kufuatia swali la msingi, Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Kilosa – Lumuma ambayo ni barabara muhimu kwa kuchukua vitunguu, iweze kupitika mwaka mzima bila ya matatizo?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali Mheshimwia Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya barabara muhimu zote katika halmashauri zetu zote kote nchini na tumewaelekeza mameneja wa TARURA katika wilaya hizo kuweka kipaumbele kwenye barabara zote muhimu kama ambayo hii ameitaja Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma. Kwa hiyo, nitoe maelekezo kwa meneja wa TARURA wa Wilaya hii ya Kilosa lakini pia wa Mkoa wa Morogoro kuhakikisha wanaipa kipaumbele barabara hii katika bajeti ili iweze kutimiza malengo ya kusafirisha bidhaa muhimu ambazo Mheshimiwa Mbunge amesema, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa barabara nyingi za ndani za TARURA ndani ya Jimbo la Kibamba zimeharibika sana na wananchi wanashindwa kufanya shughuli zao za maendeleo; je, ni upi mkakati wa Serikali kwenye kujenga barabara ya King’ong’o – Temboni - Saranga – Ukombozi - Goba – Majengo - Kwandogo – Kwashija na Luguluni – Mbokomu? Upi mkakati wa Serikali wa kukamilisha barabara hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Jimbo la Kibamba kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara nyingi za Jimbo la Kibamba zina hali mbaya na sisi kwenye bajeti ya TARURA ya mwaka ujao wa fedha tumeweka kipaumbele na bajeti imeongezeka sana ya Jimbo la Kibamba na namuelekeza pia Meneja wa Manispaa ya Ubungo kuhakikisha anazipa kipaumbele barabara za Jimbo la Kibamba ili ziweze kujengwa na kuhakikisha wananchi wanapata ahueni ya kupita katika barabara ambazo ziko bora, ahsante sana.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuunganisha kata zilizoko Mashariki na Kaskazini mwa Mlima Meru kwa kujenga barabara itakayounganisha barabara kuu ya Moshi na barabara kuu inayokwenda Namanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hizi ambazo zinaunganisha Kata za Mashariki ya Meru na Moshi na maeneo mengine yote ni miongoni mwa barabara ambazo Serikali imeweka mpango, kwanza wa kuziainisha, kuzifanyia upembuzi yakinifu, lakini kutenga bajeti kwa ajili ya kuanza ujenzi wa ukamilishaji wa barabara hizo. Lakini jambo la msingi hapa Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na Meneja wa TARURA katika Halmashauri hii ya Arusha wafanye tathmini ya barabara muhimu zaidi ambazo zinatakiwa kupewa kipaumbele ili Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hizo, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Swali langu ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga barabara kutoka Mji Mdogo wa Himo kupitia Sokoni kwenda Lotimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Mji Mdogo wa Himo ambayo inakwenda kuunganisha na miji mingine ni barabara muhimu na ni barabara ambayo tulishaelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Kilimanjaro na Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Moshi kuhakikisha kwamba wanazifanyia tathmini na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi ili Serikali itafute fedha kujenga barabara hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuwahakikishie kwamba tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya barabara hizo, ahsante.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2021 Waziri wa TAMISEMI aliahidi kujenga kituo cha afya katika Kata ya Ikuna; je, Serikali ni lini itatimiza ahadi hiyo? Swali la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika Wilaya ya Kilolo, Kata ya Ukumbi, wananchi wamejenga jingo la kituo cha afya kwa nguvu zao wenyewe na OPD imekamilika; je, Serikali iko tayari kuelekeza fedha zilizotengwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya katika Kata ya Ukumbi ili majengo yale ya vituo vya afya yaweze kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo kwa niaba ya Mheshimiwa Enosy Swalle Mbunge wa Lupembe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali tunatambua tuna commitment ya kupeleka fedha kujenga kituo cha afya cha Kata ya Ikuna, na Mheshimiwa Mbunge wa Lupembe, Mheshimiwa Edwin Swalle, amekuwa akifuatilia mara kwa mara kwa bidii sana kuhusiana na miradi ya maendeleo kwa ujumla, lakini Kituo cha Afya cha Ikuna. Nimhakikishie kwamba Serikali tayari tunatafuta fedha kwa ajili ya kwenda kujenga Kituo cha Afya cha Ikuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuhusiana na Kituo cha Afya cha Kilolo ambacho wananchi wamejenga niwapongeze sana wananchi wa Kilolo kwa kutoa nguvu zao na niwahakikishie kwamba Serikali imeweka mpango wa kuchangia nguvu za wananchi kukamilisha ujenzi wa vituo vya afya na tutafanya hivyo, ahsante.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kuwa wananchi wa Kata ya Ihanda na Msia, wametenga maeneo na wametayarisha matofali na mawe kwa ajili ya vituo vya afya.

Je, upi mkakati wa Serikali katika kuwaunga wananchi hao kuhakikisha vituo vya afya hivyo vinajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hasunga Mbunge wa Jimbo la Vwawa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mpango, kwa mwaka ujao wa fedha wa kukamilisha vituo vya afya, zahanati na hospitali za halmashauri, lakini kununua vifaa tiba kwa ajili ya kuhakikisha vituo vile vinaanza kutoa huduma na baada ya hapo sasa tuaendelea na ukamilishaji wa vituo vya afya, vikiwemo vituo vya afya vya Jimbo la Vwawa.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali, je ni lini Serikali itaanza ukarabati wa Kituo cha Afya cha Mwika, kwa kuongeza jingo la wodi ya watoto pamoja na jengo la upasuaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Kimei, amefuatilia sana suala la ukarabati wa Kituo cha Afya cha Mwika, na sisi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, tulishamhakikishia kwamba tunatafuta fedha kwa ajili ya kujenga wodi ya watoto, wodi ya upasuaji lakini pamoja na ukarabati wa kituo kile na tutafanya hivyo.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nataka kujua Kituo cha Afya Honyali, tulikipelekea shilingi milioni 250 wajenge na baada ya hapo wataongeza milioni 250 kukimalizia. Wananchi wamejitahidi kwa kupitia Halmashauri ya Bunda na wako katika hatua nzuri. Ni lini sasa hela ya pili itaenda shilingi milioni 250 ili wamalizie kituo chao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tulipeleka shilingi milioni 250 na kazi ya Ujenzi wa Kituo cha Afya inakwenda lakini masharti ni kwamba baada ya kukamilisha ujenzi wa shilingi milioni 250 ndipo shilingi milioni 250 nyingine zitapelekwa. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutapeleka mara baada ya kukamilisha matumizi ya shilingi milioni 250 ya kwanza. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, hospitali ya Mji wa Mafinga inahudumia zaidi ya halmashauri tano na pia iko kando kando ya barabara kuu ya kwenda Zambia mpaka South Africa. Kutokana na sababu hiyo imekuwa na msongamano mkubwa sana wa wagonjwa katika kutoa huduma.

Je, Serikali iko tayari kupitia basket fund, kuongeza bajeti katika Hospitali hii ya Mafinga ambayo inahudumia halmashauri zaidi ya tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Hospitali ya Mji wa Mafinga iko barabara inahudumia wananchi wengi kutoka pia kwenye kata na halmashauri za jirani, na utaratibu wa fedha za basket fund utaendelea kutolewa kulingana na population iliyoko ndani ya halmashauri husika na ndicho kinachofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la msingi nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi sasa Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan inajenga vituo vya afya katika kata zote za kimkakati na hospitali za halmashauri katika halmashauri ambazo hazina hospitali. Kwa hiyo, automatically tutapunguza wagonjwa ambao wengi wanakwenda hospitali ya Mji wa Mafinga.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Ninatambua mchango wa Mbunge wa Jimbo la Rungwe katika kuchangia Zahanati ya Kiwira, Serikali mtatuongezea lini fedha ili aweze kumalizia jengo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba wananchi wamechangia nguvu zao na kujenga Zahanati ya Kiwira na nimhakikishie Serikali imeweka mkakati ambao kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha tunafanya tathmini na kuongezea fedha na kukamilisha majengo hayo na tunafanya pia tathmini katika Zahanti hii ya Kiwira. Ahsante.

MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Mbinga Mjini mahitaji ya walimu kwenye shule za sekondari ni idadi ya 370 lakini waliopo ni 279 kuna upungufu wa walimu 91 hasa kwenye masomo ya sayansi na hesabu. Shule za msingi mahitaji ni 1,026 waliopo ni 605 upungufu 421 na ikama ya wafanyakazi katika afya wanaohitajika ni 725 waliopo ni 294 upungufu ni 431. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upungufu huu mkubwa na kwa sababu Serikali imeahidi kwamba inafanya ajira, nilitaka nijue, je, Naibu Waziri ananihakikishia kwamba katika mgao huo wa watumishi, jimbo langu litapata watumishi wa kutosha ili kuweza kuziba hilo pengo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, katika maelezo ya Serikali na mkakati uliopo ni kujenga vituo vingi vya afya nchini. Lakini Serikali haijaonesha kwamba kuna mkakati gani wa dharura wa kuajiri watumishi ili kuhakikisha kwamba tunaziba hili pengo la wafanyakazi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na upungufu wa watumishi wa sekta zote, sekta ya elimu na sekta ya afya naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeweka mikakati ya dhati na inatekelezwa ya kuajiri watumishi wa elimu na watumishi wa afya na ndiyo maana hivi sasa tunapoongea tunaajira ambazo zinaendelea kuchakatwa za maombi ya watumishi ambao watapelekwa kwenye vituo vyetu vya afya lakini pia kwenye elimu na tutaendelea kufanya hivyo. Ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Nkenge – Misenyi tunaishukuru Serikali kutujengea vituo vya afya vya Kanyigo, Kakunyu na Kabyaile. Je, ni lini Serikali itatupelekea watumishi wa afya katika vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Semuguruka amekuwa akifuatilia sana suala la watumishi katika vituo hivyo na nimhakikishie kwamba Serikali kama ilivyoanza kuajiri sasa tutahakikisha tunaendelea kuajiri, lakini pia kupeleka watumishi katika vituo hivyo. (Makofi)

MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, shida iliyopo Mbinga Mjini inalingana sawasawa na Mbinga Vijijini kwa wahudumu wa afya tulitakiwa kuwa nawatumishi 751 waliopo ni 210 tu tuna upungufu zaidi ya asilimia 80. Je, Serikali ipo tayari angalau kupunguza upungufu wa watumishi huu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Kapinga nimhakikishie kwamba tunafahamu kuna upungufu wa watumishi wa afya lakini pia wa elimu katika Halmashauri ya Mbinga Vijijini na mkakati ni kwamba kufuatia tathimini yetu halmashauri zile zenye upungufu mkubwa zaidi kama Mbinga Vijijini tutaleta watumishi wa kutosha zaidi, ahsante. (Makofi)
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kwanza kabisa kuuliza swali la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Hospitali ya Wilaya ya Singida Vijijini, inakabiliwa na ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa. Je, ni lini Serikali itapeleka gari katika hospitali hii ili kuokoa vifo vya kinamama wajawazito na watoto?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kituo cha afya cha Sepuka, kiko pembezoni na hakina gari la kubebea wagonjwa. Je, ni lini Serikali itapeleka gari katika kituo hiki cha afya?

Mheshimiwa Spika, ninakushukuru.(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kwali kwamba ni kweli kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Singida Vijijini inahitaji gari la wagonjwa na Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuwajali wananchi wote katika Halmashauri zetu kote nchini itapeleka magari ya wagonjwa ndani ya mwaka huu wa fedha au mapema mwaka ujao wa fedha ikiwemo Halmashauri ya hii ya Singida Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Sepuka ambacho kiko pembezoni, tumefanya tathmini ya kuona vituo ambavyo viko pembezoni ambavyo vinahitaji magari ya wagonjwa vitapelekewa magari ya wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, amekuwa akifuatilia sana masuala ya maendeleo ya wananchi wa Mkoa wa Singida na Watanzania kwa ujumla nimhakikishie kwamba tutaendelea kumpa ushirikiano. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Nataka nimuulize swali Naibu Waziri, kuna Halmashauri zingine zina Majimbo zaidi ya mawili au matatu, sasa kama mtapeleka gari moja, hilo gari litaenda kwenye Jimbo gani? Kwa nini usiweke wazi, kwa nini isiwe kwa Majimbo badala ya kuwa Halmashauri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa kupeleka magari ya wagonjwa kwenye Halmashauri unazingatia vigezo, kigezo cha kwanza ni idadi ni ya watu katika Halmashauri, kigezo cha pili ni idadi ya wagonjwa kwa maana ya burden of disease katika Halmashauri husika. Utaratibu huu hauzingatii Majimbo kwa sababu Majimbo pia yanatofautiana na idadi ya wananchi ukilinganisha na Halmashauri. Kwa hiyo, tutakwenda kupeleka magari haya, kwa kigezo cha Halmashauri na idadi ya watu na burden of disease. Pale ambapo itahitajika kwa Majimbo mawili kupata gari tutafanya hivyo. (Makofi)
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, pamoja na hivyo naomba niulize maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa wananchi wa Ludewa wamevuja jasho sana kuanza ujenzi kwenye Kata 12, Je, ni lini Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuambatana na mimi ili kwenda kushuhudia jinsi wananchi walivyojitoa kutoa kujenga vituo vya afya na havijamaliziwa na Serikali?

Swali la pili, kwa kuwa Tarafa ya Mwambao haina usafiri wa magari na meli kwa muda mrefu haipo. Je, ni kwanini Serikali isitafute boti moja ya mwendokasi ambayo itasaidia wagonjwa kuanzia Lumbila, Kilondo, Makonde, Lifuma, Mkali mpaka Manda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Kamonga, amekuwa akifuatilia sana miradi ya maendeleo kwa ajili ya wananchi wa Jimbo la Ludewa, ikiwemo vituo vya afya na magari ya magonjwa. Kwa kweli katika Kata hizi 12 ambazo wananchi wamechangia nguvu zao kujenga vituo vya afya, nimhakikishie kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuunga mkono juhudi za wananchi kukamilisha vituo hivi.

Mheshimiwa Spika, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa, kwa mwaka ujao wa fedha baada ya mwaka huu ambao tumeshaupangia bajeti atenge fedha kwa ajili ya kujenga maabara na kichomea taka kwenye vituo ambavyo wananchi wameshaweka nguvu zao, ili huduma za OPD zianze na Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha vituo hivyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na ambulance, boti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafanya tathmini maeneo yote ambayo ni magumu kufikika ya visiwa na ambayo yanapitiwa na mikondo ya maji, tuangalie uwezekano wa kupata ambulance hizi za boti kwa kadri ya upatikanaji wa fedha na tutatoa kipaumbele kwenye Wilaya ya Ludewa.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kufahamu ni lini Serikali itatujengea Kituo cha Afya, katika Kata ya Bara ili kupunguza idadi ya vifo vya mama na mtoto katika Wilaya ya Mbozi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeandaa mkakati, kwanza wa kukamilisha vituo vyote zahanati na hospitali za Halmashauri ambazo zimekamilika lakini hazijaanza kutoa huduma. Baada ya hapo tutakwenda sasa kujenga vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati likiwemo eneo hili ambalo Mheshimiwa Juliana Shonza amelisema.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tutakwenda kuhakikisha kwamba tunajenga pia kituo cha afya baada ya kukamilisha vituo vingine.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya katika Kata ya Miula Jimbo la Nkasi Kusini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaweka mkakati wa kuainisha maeneo ya kujenga vituo vya afya, ikiwemo katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, kwa hivyo, kadri ya upatikanaji wa fedha katika bajeti inayofuata tutahakikisha tunatenga fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo hayo. Ahsante.

MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 kuna Kata ya Tumbi pamoja na Kata ya Misha tayari vituo vya afya vimeashaanza kujengwa na vipo katika hali ile ya kumalizia. Ni lini Serikali italeta fedha hizi za kumalizia vituo hivyo vya afya viwili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba kata nyingi bado zinahitaji vituo vya afya, lakini Kata za mkakati tumekwishaziainisha na Waheshimiwa Wabunge, walileta Kata za kipaumbele tatu kila Jimbo, niwahakikishie kwamba Serikali inaendelea kuandaa bajeti kwa ajili ya kuendelea na ukamilishaji wa vituo hivi vya afya, vikiwemo hivi vituo vya afya viwili ambavyo vipo katika Jimbo la Tabora Mjini.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Serikali ndiyo ilihamasisha ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo mbalimbali nchi nzima na kuwahamasisha wananchi washiriki lakini leo hazijakamilisha. Je, mliamua kuwahamasisha wananchi bila kuwa na fedha za kutosha ndiyo maana kila Mbunge leo anaulizia kituo cha afya. Kwa nini sasa msikamilishe wakati ninyi ndiyo mliwahamasisha wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tukubaliane kwamba kuhamasisha wananchi kuchangia nguvu zao katika ujenzi wa vituo vya afya ni dhamira njema na jambo jema kwa sababu wananchi wetu wamekuwa wanasafiri umbali mrefu sana kupata huduma za afya. Kwa hiyo, kwa kuanza tu jambo hilo lilikuwa ni jema na nia njema ya Serikali lakini tumeendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma.

Mheshimiwa Spika, mwaka uliopita maboma 555 ya zahanati Bilioni 33.5 zilipelekwa, mwaka huu tumepeleka katika maboma zaidi ya 234 ya vituo vya afya na zahanati. Mwaka ujao tunayo maboma 300 ya zahanati ambayo yanakwenda kukamilishwa. Kwa hiyo, Serikali inafanya kazi ya kukamilisha maboma hayo kwa nia njema ya kusogeza huduma kwa wananchi, lakini safari ni hatua, tutakwenda kwa awamu mpaka kukamilisha majengo hayo yote. (Makofi)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Lazaro Londo, inaonekana fedha ambayo imetengwa kwa ajili ya barabara hiyo haitoshi. Sasa ni nini comment ya Serikali kuhakikisha kwamba barabara hiyo inatengewa fedha za kutosha ili iweze kujengwa na kukamilika na wananchi waitumie?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, barabara hii ya Kisanga, Malolo na Uleling’ombe ni barabara ambayo inatumika kama barabara mbadala kipindi barabara ya kwenda Iringa ya lami inapokuwa ina hitilafu. Je, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba barabara hii inatengenezwa na inatumika kipindi chote cha mwaka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. NDUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo yaliyoulizwa na Mheshimiwa Florent Kyombo kwa niaba yake kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii lakini fedha haitoshi. Kimsingi tunafahamu kwamba safari ni hatua, tunaanza na hatua moja tunakwenda na hatua nyingine, angalau Serikali imeanza kuweka fedha, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kutafuta fedha kukamilisha barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na hii barabara nyingine ambayo inaunganisha maeneo haya muhimu ya Kata hizi mbili ya Kisanga na Uleling’ombe nayo iko kwenye mpango. Nimeeleza hapa na tutahakikisha kwamba tunaendelea kutafuta fedha kujenga barabara hizi kadri ya upatikanaji huo. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kufuatia swali la msingi, Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya Kilosa – Lumuma ambayo ni barabara muhimu kwa kuchukua vitunguu, iweze kupitika mwaka mzima bila ya matatizo?

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali Mheshimwia Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imefanya tathmini ya barabara muhimu zote katika halmashauri zetu zote kote nchini na tumewaelekeza mameneja wa TARURA katika wilaya hizo kuweka kipaumbele kwenye barabara zote muhimu kama ambayo hii ameitaja Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma. Kwa hiyo, nitoe maelekezo kwa meneja wa TARURA wa Wilaya hii ya Kilosa lakini pia wa Mkoa wa Morogoro kuhakikisha wanaipa kipaumbele barabara hii katika bajeti ili iweze kutimiza malengo ya kusafirisha bidhaa muhimu ambazo Mheshimiwa Mbunge amesema, ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa barabara nyingi za ndani za TARURA ndani ya Jimbo la Kibamba zimeharibika sana na wananchi wanashindwa kufanya shughuli zao za maendeleo; je, ni upi mkakati wa Serikali kwenye kujenga barabara ya King’ong’o – Temboni - Saranga – Ukombozi - Goba – Majengo - Kwandogo – Kwashija na Luguluni – Mbokomu? Upi mkakati wa Serikali wa kukamilisha barabara hizi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtemvu, Mbunge wa Jimbo la Kibamba kama ifutavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara nyingi za Jimbo la Kibamba zina hali mbaya na sisi kwenye bajeti ya TARURA ya mwaka ujao wa fedha tumeweka kipaumbele na bajeti imeongezeka sana ya Jimbo la Kibamba na namuelekeza pia Meneja wa Manispaa ya Ubungo kuhakikisha anazipa kipaumbele barabara za Jimbo la Kibamba ili ziweze kujengwa na kuhakikisha wananchi wanapata ahueni ya kupita katika barabara ambazo ziko bora, ahsante sana.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuunganisha kata zilizoko Mashariki na Kaskazini mwa Mlima Meru kwa kujenga barabara itakayounganisha barabara kuu ya Moshi na barabara kuu inayokwenda Namanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara hizi ambazo zinaunganisha Kata za Mashariki ya Meru na Moshi na maeneo mengine yote ni miongoni mwa barabara ambazo Serikali imeweka mpango, kwanza wa kuziainisha, kuzifanyia upembuzi yakinifu, lakini kutenga bajeti kwa ajili ya kuanza ujenzi wa ukamilishaji wa barabara hizo. Lakini jambo la msingi hapa Mheshimiwa Mbunge kushirikiana na Meneja wa TARURA katika Halmashauri hii ya Arusha wafanye tathmini ya barabara muhimu zaidi ambazo zinatakiwa kupewa kipaumbele ili Serikali itenge fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi wa barabara hizo, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii. Swali langu ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kujenga barabara kutoka Mji Mdogo wa Himo kupitia Sokoni kwenda Lotimu?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii ya Mji Mdogo wa Himo ambayo inakwenda kuunganisha na miji mingine ni barabara muhimu na ni barabara ambayo tulishaelekeza Meneja wa TARURA wa Mkoa wa Kilimanjaro na Meneja wa TARURA wa Halmashauri ya Moshi kuhakikisha kwamba wanazifanyia tathmini na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi ili Serikali itafute fedha kujenga barabara hizo. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tuwahakikishie kwamba tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya barabara hizo, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza ni kwamba, wakati wa bajeti tarehe 26 Machi, 2022 kwenye Kamati ya TAMISEMI, waliahidi wataalam kwamba watapeleka fedha hizi tarehe 30 Machi. Leo Waziri anasema tarehe 30 Mwezi Juni, maana yake miezi mitatu baadaye. Kama hii kauli ya mwanzo iliahidi Kamati ya Fedha, fedha haijaenda mpaka leo tunavyozungumza, tarehe 30 Juni, fedha itaenda kweli?

Swali la kwanza, fedha hiyo inaenda lini Ili iweze kujenga kituo cha afya pale? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; hapo Hospitali ya Mwaga ilikuwa ni zahanati kama kituo cha afya, sasa ni Hospitali ya Halmashauri mpya, hakuna mgao wa dawa pale, lakini hizi huduma ninazozizungumza wodi ya akinamama haijakamilika, wodi ya watoto haijakamilika, wodi ya wanaume haijakamilika, pharmacy haijakamilika, fedha ipo milioni 78 kwenye mgodi wa North Mara, Mheshimiwa Waziri wa Madini aliagiza kwamba ndani ya siku 14 fedha iende haijaenda, Waziri wa TAMISEMI aliagiza fedha haijaenda...

SPIKA: Mheshimiwa Mwita Waitara, ngoja kwanza. Jibu la msingi la Waziri, wewe kwa hilo swali lako la pili unalotaka kuuliza ni kwamba, hili jibu lake la msingi halitoi uhalisi wa kilichoko huko ndiyo unachojaribu kusema? Simama.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ni kweli.

SPIKA: Kwa hiyo, hakuna hizo wodi mbili zilizokamilika.

MHE. MWITA M. WAITARA: Hazijakamilika.

SPIKA: Basi hilo swali lako la nyongeza la kwanza nitampa nafasi Mheshimiwa Waziri alijibu, hilo la pili unalosema hayo majibu hayako halisi Mheshimiwa Naibu Waziri atakapomaliza kujibu maswali hapa, nitampa nafasi aende akalifuatilie aniletee majibu hapa.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Waitara, Mbunge wa Jimbo wa Tarime Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Halmashauri ya Tarime Vijijini walitakiwa kupeleka milioni 100 lakini hawakupeleka milioni 100 katika kata hii kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo cha afya tarehe 30 Machi na jana nimewasiliana na Mkurugenzi na Katibu Tawala wa Mkoa na watapeleka ndani ya mwezi huu kwa sababu walikuwa hawajapata makusanyo ya kutosha kupeleka fedha hiyo kwa mujibu wa vipaumbele ambavyo vilikuwa vimewekwa. Ahsante sana.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Lutende, mwaka 2019 walipeleka shilingi bilioni 200 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya na jengo la OPD limekamilika. Palikuwa pana ongezeko la milioni 300 lakini kata hiyo haijapelekewa fedha hiyo. Je, ni lini watapeleka fedha hiyo ili tuweze kumaliza Kituo cha Afya cha Kata ya Lutende?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nnaomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kituo hiki kilipelekewa milioni 200 na kama ilivyo kwa vituo vyote ambavyo vilipelekewa milioni 200 au milioni 250, awamu inayofuata wanapewa milioni 300 au milioni 250 kukamilisha milioni 500 ili kukamilisha vituo vya afya. Kwa hiyo, fedha hiyo itapelekwa kwenye kituo hicho cha afya. Ahsante.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kata ya Miluwi iko umbali wa kilomita 80 kutoka Liwale Mjini ambako kuna hospitali ya wilaya na uhitaji wa kituo cha afya pale ni mkubwa sana na wananchi wameshaanza ujenzi wa kituo cha afya pale. Je, Serikali iko tayari kusaidia kwenye bajeti hii kuunga mkono juhudi zile za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, Mbunge wa Jimbo la Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze sana wananchi wa Kata hii ya Miluwi ambao wameanza kuchangia nguvu zao kujenga kituo cha afya na niwahakikishie kwamba Serikali itaendelea kuchangia katika hizo nguvu za wananchi ili kuhakikisha kwamba kituo hicho kinakamilika kwa awamu. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Wananchi wa Kata ya Dalai walijihamisha wakaanza ujenzi wa kituo cha afya. Lini sasa Serikali nayo itaweka nguvu zao ili kituo kile kimalizike? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa sababu wananchi wameanza ujenzi wa kituo cha afya kwa nguvu zao, tumewapongeza kwa juhudi hizo, lakini Serikali itaendelea kutafuta fedha kama ilivyo kwa majimbo mengine yote ili kuchangia nguvu za wananchi kukamilisha vituo ambavyo vimeanza ujenzi. Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Mbunge awe na subira kwamba Serikali inatambua hilo na italifanyia kazi. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Zahanati za Tandika pamoja na Mibulani zitaanza kufanya kazi kwa sababu majengo yako tayari na kila kitu na yameanza kupata ufa, tusiipoteze Serikali fedha zile. Je, ni lini zitaanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, vituo vyote vilivyokamilika vinatakiwa vianze kutoa huduma mapema iwezekanavyo na natoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke kuhakikisha zahanati au vituo hivi vya Tandika na Mibulani vinasajiliwa haraka iwezekanavyo na vinaanza kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyotarajiwa.
MHE. GHATI Z. CHOMETE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Kwa kuwa miradi ya TACTIC, imeshaanza na Halmashauri ya Manispaa ya Mji wa Musoma haimo kwenye miradi hiyo kwa sasa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha mradi huo unaanza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Stendi ya Mabasi ya Mji wa Musoma ina hudumia wananchi kutoka Tarime, Serengeti, Rorya, Butiama, Musoma Vijijini na maeneo mengine yanayozunguka Mkoa wa Mara. Kwa sasa stendi ile ni chakavu sana na haipitiki hasa mvua ikinyesha. Je, Serikali ina mkakati upi wa muda mfupi, kuhakikisha stendi ile inaendelea kuingilika ili kusubiri mkakati wa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Miradi ya TACTIC, itaanza utekelezaji wake rasmi mwaka wa fedha 2022/2023, lakini Halmashauri hii ya Musoma pia ipo kati ya zile lot ya kwanza, ya pili na ya tatu ambapo tutakwenda kutekeleza. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba itapokuwa inaanza mwaka ujao wa fedha, basi Manispaa hii ya Musoma hii stendi itakuwa miongoni mwa zile lot tatu ambazo zipo kwenye TACTIC.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na Stendi ya Mabasi ya Musoma Mjini kuwa ni chakavu sana na inahudumia wananchi wengi. Natoa maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Musoma kuhakikisha wanatenga fedha za mapato ya ndani, kwa sababu stendi ni kipaumbele lakini ni chanzo cha mapato. Kwa hiyo, lazima mapato ya ndani yaanze kuboresha stendi ile wakati wanaandaa andiko la kuomba fedha kama mradi wa mkakati kwa ajili ya kukamilisha. Ahsante.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Wananchi wa Mkoa wa Rukwa wanateseka sana kuhusiana na stendi, stendi iko mbali na stendi ya zamani iko mjini. Je, ni lini sasa Serikali itaruhusu wananchi wa Mkoa wa Rukwa watumie stendi zote mbili kama inavyotumia Mkoa wa Mbeya, wanashusha Uyole, wanashusha Nane Nane na wanashusha stendi ya zamani. Hivyo, ni lini sasa Serikali itaruhusu wananchi wa Rukwa watumie stendi ya zamani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maamuzi ya mkoa kwa maana ya Viongozi wa Mkoa; Mkuu wa Mkoa, Katibu Tawala na Menejimenti za Halmashauri zetu zote, nawaelekeza wakae wafanye tathmini kwamba kwa nini stendi ya zamani haitumiki na inatumika stendi mpya ambayo iko mbali na waone uwezekano wa kufanya maamuzi stendi ipi itumike au zitumike zote na watupe mrejesho Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo, suala hilo litafanyiwa kazi na Serikali. Ahsante.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Ni muda mrefu sasa katika Mji wa Babati hatuna stendi na stendi haijamaliziwa. Je, ni lini Serikali italeta fedha ili ujenzi ule wa stendi ya Babati ukamilike kama ulivyoahidiwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Regina Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa stendi na miradi mingine yote ya kimkakati, kwanza ni jukumu la halmashauri kuainisha gharama, lakini pia kuwasiliana na Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kuona kwanza kama wana uwezo wa kuzijenga kupitia mapato ya ndani, lakini pili kama wanahitaji kupata fedha kutoka Serikali. Kwa hiyo, mamlaka ya Halmashauri ya Babati, ilete taarifa ya mpango wa utekelezaji wa stendi ile ili Serikali tuone namna ya kufanya, kama watajenga kwa mapato ya ndani au kama tutafuta fedha kwa ajili ya kujenga kama mradi wa kimkakati. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwa kuwa stendi ya mabasi ya Shinyanga Manispaa imechakaa na ni ya zamani haijajengwa kisasa, je, ni lini Serikali itajenga Stendi Kuu ya Mabasi, Manispaa ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, stendi hizi zote kama nilivyotangulia kujibu kwenye jibu la awali la halmashauri husika, Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, wafanye tathmini na kuona gharama ambazo zinahitajika kukamilisha au kujenga stendi ile, lakini waone uwezo wao wa mapato ya ndani kutenga kwenye bajeti. Kama inahitaji gharama kubwa, walete andiko hilo Ofisi ya Rais, TAMISEMI, ili tuweze kufanya tathmini na kutafuta vyanzo vya fedha. Ahsante.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali ina mkakati gani wa kufanya ulezi kwa vikundi hivi si tu vya vijana lakini vikundi vya wanawake na watu wenye ulemavu, ili viweze kuwa na ufanisi katika kufanya shughuli zake za ujasiriamali?

Swali langu la pili, tathmini inaonesha kwamba malipo ya fedha hizi za mikopo zinazotoka kwenye Halmashauri bado zinasuasua. Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba mikopo hii inalipwa kwa wakati ili waweze kunufaika vijana wanawake na watu wenye ulemavu wengi zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zainab Katimba Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati ambao Serikali imekuwa inaufanyiakazi katika kuhakikisha vikundi hivi ambavyo vinakopeshwa wajasiliamali wadogo wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kuwa endelevu lakini pia kuweza kuwa na tija ni Maafisa Maendeleo ya Jamii katika Halmashauri husika kwanza kuwatembelea mara kwa mara, kuwafanyia mafunzo ya mara kwa mara, pia kuwashauri kuona kwamba wanakwenda vizuri na huo ndiyo ulezi wenyewe kwa maana ya kwamba viongozi wa Halmashauri lakini katika ngazi za Kata, Waheshimiwa Madiwani na Viongozi wengine wanahusika kuvifuatilia pia kuvishauri. Tutaendelea kufanya hivyo ili kuhakikisha kwamba vikundi hivi vinakopa lakini vinarejesha kwa tija.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na malipo ya fedha kusuasua ni kweli, kumekuwa na changamoto kwa baadhi ya Watendaji kuchelewesha malipo haya na Serikali ilishatoa maelekezo kwamba kama kikundi kina kinakidhi vigezo kipate fedha mapema iwezekanavyo ili shughuli ziweze kuendelea, lakini mara nyingine zinacheleweshwa kutokana na baadhi ya vikundi kutokidhi vile vigezo vinavyotakiwa. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini kwa mujibu wa sensa ya mwaka 2012 tuna idadi ya watu wenye ualbino wapatao 16,000 lakini kutokana na jibu la Serikali inaonesha kwamba watu wenye ualbino ambao wamenufaika na mafuta haya ni 3,389 kwa kipindi cha mwaka 2020 hadi 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tukumbuke kwamba Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI alishatoa maelekezo kwa Halmashauri hizi kwamba zihakikishe zinanunua na kugawa mafuta haya ya watu wenye ualbino.

Nini kauli ya Serikali kwa Halmashauri ambazo hazitatekeleza takwa hili, na hasa ikizingatiwa kwamba maelekezo yameshatolewa mara nyingi, lakini pia miongozo ipo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili la nyongeza; kwa kuwa sasa hivi tunakwenda kuwa na zoezi hili la sensa, hivyo tunategemea kwamba tutapata idadi halisi ya watu wenye ulemavu, aina za ulemavu na mahali wanapopatikana ama mahali walipo.

Serikali inaonaje sasa ikianza kuyanunua mafuta haya ikawa inayashusha moja kwa moja kwenye vituo vya afya na zahanati, tofauti na utaratibu uliopo sasa ambapo mafuta haya kwa maeneo ambayo yalikuwa yakinunuliwa yalikuwa yakipatikana kwenye Hospitali za Mikoa na Wilaya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Stella Ikupa amekuwa mstari wa mbele sana kuhakikisha anawasemea watu wenye ulemavu wakiwemo wenye ulemavu wa ngozi na Serikali ya Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, inawajali na kuwathamini sana watu wote wenye ulemavu na ndiyo maana katika mipango yetu tumekubaliana kwamba kwanza ni maelekezo ya Serikali kwamba Halmashauri zetu zote zinapotenga fedha kwa ajili ya dawa lazima zitenge fedha kwa ajili ya mafuta haya kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa ngozi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kurudia tena kauli hiyo ya Serikali ambayo ilikwishatolewa kwamba Halmashauri zote zihakikishe zinatenga fedha, miongoni mwa bajeti ya dawa lazima mafuta haya ya watu wenye ualbino yaweze kuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari kwenye bajeti ya mwaka 2022/2023 Halmashauri zote zimefanya utambuzi na kufanya maoteo ya mahitaji ya mafuta hayo na katika mwaka huu tutakuwa na mafuta hayo kwa kiasi kikubwa zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuhusiana na kusogeza huduma hizi karibu zaidi na watu wenye ulemavu, ni kweli tutakuwa na Sensa ya Watu na Makazi tarehe 23 Agosti, 2022. Niwaombe watu wote wenye ulemavu, pamoja na Watanzania wote, tujitokeze wote ili tuhesabiwe, na hii itasaidia sana Serikali kuwatambua watu wenye ulemavu na kujua mahali walipo na mafuta haya sasa yatasogezwa kwenye vituo vile kwa idadi kulingana na watu wenye ulemavu walipo katika maeneo hayo, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante; kwa kuwa watu wengi wenye ulemavu wa ngozi hawako kwenye vituo, wengine wako vijijini; je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba hata wale ambao hawko kwenye vituo vya Watoto walio na albinism.

Je, nini mkakati wa Serikali kuwafikia kule waliko kuwapa mafuta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba siyo wote wenye ulemavu wa ngozi (ualbino) wapo kwenye vituo vya huduma, kwa maana ya watoto, lakini hapa tunaongelea watoto na watu wazima kupata huduma hii. Sasa utaratibu ambao tutauweka, kwanza tukisogeza huduma hizi za mafuta karibu na zahanati na vituo maana yake wale watu wenye ualbino watajua kwamba mafuta yakiisha watakwenda kwenye zahanati ya karibu zaidi au kwenye kituo cha afya au hospitali ya karibu zaidi. Kwa hiyo, mpango wa Serikali ni kusogeza zaidi upatikanaji wa huduma hii kwenye vituo katika jamii zetu, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, Kituo cha Afya cha Namiungo, ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Magufuli ambaye ni Hayati, alitoa ahadi Milioni 500 ili kuweze kukamilisha Kituo cha Afya cha Namiungo. Sasa je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi hiyo ya Mheshimiwa Rais?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Kituo cha Afya cha Nakapanya, kilitengewa fedha kiasi cha shilingi milioni 400 mwaka wa fedha 2021 na kilipokea shilingi milioni 200 na kujenga majengo ya upasuaji pamoja na maabara.
Je, ni lini Serikali itatupatia kiasi kilichobaki ili kuweza kujenga majengo mengine muhimu kama vile mortuary na mionzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeza sana Mheshimiwa Kungu kwa namna ambavyo anawakilisha kwa dhati wananchi wa Tunduru Kaskazini, na nimhakikishie kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kipaumbele cha Serikali. Tunafahmu kwamba Namiungo ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, nasi tayari tumeshaweka mpango wa kupata fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Namiungo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Nakapanya, hiki ni kituo kati ya vituo 52 ambavyo katika mwaka wa fedha huu tumetenga Bilioni 15.6 kwa ajili ya umaliziaji wa vituo hivi kikiwemo kituo hiki cha afya cha Nakapanya. Ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Je, ni lini Serikali itapeleka Shilingi Milioni 200 katika Kituo cha Afya cha Nyalioba, ikiwa ni ni utekelezaji wa ahadi ya Makamu wa Rais, Dkt. Philip Isdor Mpango?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Florence Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samizi anawasemea sana wananchi wa Jimbo la Muhambwe, nakumbuka katika ziara ya Mheshimiwa Makamu wa Rais tulikuwa pamoja tuliahidi Milioni 200 Mheshimiwa Makamu wa Rais aliahidi. Ninakuhakikishia kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI tayari imetenga fedha hizo na wakati wowote zitaingia kwenye Kituo cha Afya cha Nyalioba, ahsante.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. Mheshimiwa Hayati Dkt. Magufuli mwaka 2018 aliahidi kutoa Shilingi Milioni 100 kumalizia Kituo cha Afya cha Mchomoro, lakini mpaka leo fedha hizo hazijapatikana. Je, Serikali iko tayari kuzitoa fedha hizo ili kuendeleza Kituo cha Afya cha Mchomoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Jimbo la Namtumbo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza sana Mheshimiwa Kawawa kwa kazi kubwa anayofanya kuwasemea wananchi wa Namtumbo, na nimhakikishie kwamba ahadi ya Mheshimiwa Rais ni kipaumbele, tunafahamu milioni 100 inahitajika katika kituo hiki cha Namchomoro na tutaleta fedha hiyo kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho. Ahsante.

MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mwaka jana Wabunge wote tulitoa vipaumbele vya vituo vya afya kwenye Kata mbalimbali nchini. Je, ni lini Serikali itatupatia fedha za Kituo cha Afya cha Kata ya Ruvu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mwakamo, amekuwa mchapakazi sana, mwakilishi mzuri wa wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, tunafahamu kwamba Kata ya Ruvu inahitaji kituo cha afya, kwa sasabu ya idadi ya wananchi waliopo na tayari tumeweka kwenye mpango mkakati kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Ruvu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ucheleweshaji sio la Biharamulo, kwa sababu Biharamulo walishawasilisha Mkoani na Mkoani wanaleta moja kwa moja TAMISEMI. Jengo la Halmashauri ya Biharamulo, liko kwenye miradi ya kimkakati ya Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa. Swali la kwanza, maombi yalikuwa ni bilioni 3.4 lakini Serikali imetenga bilioni 2.7 kwa mwaka wa fedha 2023/2024 lakini kwa uchumi wa Biharamulo haitaweza kupata hiyo milioni 700 inayosalia.

Je, Serikali ina mpango gani waku-top up kiasi hicho cha fedha tukifika wakati huo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali tayari imeshaweka commitment na ahadi kwamba itatenga hiyo bajeti ya bilioni 2.7; je, bado kuna haja tena ya kuandika maombi haya au hakuna haja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Neema Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum ambayo ameuliza kwa niaba ya Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la msingi bila kujali vimechelewa wapi ni suala la kwamba jengo la utawala la Halmashauri litatengwa kwenye mwaka wa fedha 2023/2024. Lakini kiasi ambacho kimeombwa ni Bilioni 3.475 lakini mpango wa Serikali tumefanya standardization ya majengo yetu yote ya halmashauri ili kuepukana na variation ya majengo ambayo yamekuwa yanajengwa kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kwa sasa Halmashauri zote zitakuwa na mchoro mmoja na kila halmashauri itapata bilioni 2.7, kwa hiyo hatuna haja ya kuongeza fedha hiyo, hiyo ndiyo fedha kulingana na mchoro huo ili kuhakikisha kwamba tunakuwa na standardization. Lakini pale ambapo tutalazimika kuwa na variation ya mchoro kulingana na mazingira, basi tutaona namna ya kufanya.
MHE. MUHARAMI S. MKENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumuuliza swali la nyongeza Mheshimiwa Waziri. Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo, wafanyakazi wake wanakaa sehemu tofauti tofauti, kutokana na uchakavu wa jengo, na jengo kuwa na nafasi ndogo. Je, ni lini Serikali itatujengea jengo jipya na maombi tulishapeleka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Muharami, Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kujenga majengo haya ya utawala, mpaka sasa takribani jumla ya Bilioni 224.5 zimetumika kwa majengo ya Halmashauri 95, tunafahamu Bagamoyo mlileta maombi hayo, nikuhakikishie kwamba tunaendelea kutafuta fedha na baada ya hapo tutaanza shughuli za ujenzi wa jengo la Halmashauri. Ahsante. (Makofi)
MHE. SELEMANI J. ZEDI: Mheshimiwa Spika, ahsante, nashukuru sana kwa jibu zuri sana lililotolewa na Mheshimiwa Waziri na nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali ya Awamu Sita, chini ya Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea na kutupatia shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya pale Sojo Igusule.

Mheshimiwa Spika, sasa swali langu ni kwamba Mheshimiwa Waziri, utakuwa tayari baada ya Bunge hili la bajeti uongozane na mimi kwenda Kijiji cha Sojo ili wananchi wa Sojo Igusule wakakushukuru kwa kutupatia shilingi milioni 500 za kujenga kituo cha afya ambacho tulikuwa tunakihitaji sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Zedi amekuwa akifuatilia sana juu ya ujenzi wa kituo hiki cha afya na Serikali sikivu ya Awamu wa Sita, inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan, imewasikia wananchi wa Jimbo la Bukene, na kituo hicho kitakuja na niko tayari kuongozana nawe kwenda Sojo ili wananchi waweze kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa ajili ya kutoa fedha kwa ajili ya kituo cha afya hicho. Ahsante. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mchakato wa upandishaji hadhi wa zahanati zetu kwenda vituo vya afya unafanywa na Wizara; je, Wizara haioni sasa mchakato huu mkaziachia Sekretarieti za Mikoa ifanye kazi hiyo kwa vigezo vilevile ili kupunguza huo urasimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilai Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upandishaji hadhi wa zahanti kuwa vituo vya afya au kuwa hospitali za Halmashauri unafanya na Wizara kwa kushirikiana na Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa ambapo Halmashauri wanafanya tathmini kulingana na vigezo, wanawasilisha mikoani kwa RAS na wanawasilisha Wizara ya Afya, lakini pia Ofisi ya Rais – TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utaratibu huu ni shirikishi haifanyi Wizara pekee yake ni ngazi zote zinahusika na tutaendelea kufanya hivyo kwa sababu ndiyo maana ya D by D. Ahsante sana.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, kwanza nakushukuru kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa nimeliuliza hili swali mara mbili hapa Bungeni na majibu ya Serikali yamekuwa kwamba Halmashauri bado haijawasilisha andiko; na kwa kuwa tayari Waziri ana taarifa kwamba kuna andiko ambalo limeshaandikwa, lakini limechukua muda mrefu.

Sasa je, nini kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba inaweka mkakati wa kuzisaidia Halmashauri zote nchini ambazo zinahitaji kuja na hii miradi ya kimkakati ili ziwasilishe hii miradi kwa wakati?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, Waziri yupo tayari kuambatana nami kwenda katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni ili akajionee hali halisi ya stendi ya mabasi ambayo ipo? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Dkt. Chaya amekuwa akifuatilia sana sana miradi ya maendeleo kwa wananchi wa Jimbo la Manyoni Mashariki ikiwemo stand hii na ni kweli ameuliza hapa mara pili. Na nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kwamba andiko hili limekuwa likisubiriwa kwa muda mrefu na sasa tunatoa maelekezo kwa tarehe hiyo ambayo wameji-comment tarehe 30 Juni, lazima andiko liwe limefikishwa hapa ili Serikali ifanye tathmini na kuona namna ya kuwaletea wananchi wa Manyoni maendeleo.

Mheshimiwa Spika, niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge kwenda Manyoni, tutakubaliana baada ya Bunge hili tuweze kwenda kuona stand hiyo.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Katika Manisapaa ya Mtwara Mikindani, stand ya mabasi makubwa iliyopo eneo la Chipuputa hali ya miundombinu yake ni mbaya, mvua ikinyesha maji yanajaa wasafiri wanapata shida. Nataka kujua tu kauli ya Serikali, watarekebisha lini ili stand ile iweze kutumika kwa matumizi ambayo yamekusudiwa? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tunza Malapo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Tunza kwa kufuatilia maendeleo ya wananchi wa Mtwara, lakini nimhakikishie kwamba tumetoa maelekezo kwa Wakurugenzi wote wa Halmashauri zetu kuhakikisha yale maeneo ambayo ni vipaumbele ambayo yanagusa moja kwa moja maslahi ya wananchi zikiwemo stand, kufanya tathmini kuona uwezekano wa kufanya matengenezo kwa kufanya mapato ya ndani au kuandika maandiko maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Mtwara Mikindani kufanya tathmini hiyo au kufanya matengenezo au kuleta maombi kwa ajili ya kufanya kupitia Serikali Kuu. Ahsante.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mbogwe inazo stand mbili, lakini hali yake ni mbaya sana hasa mvua ikinyesha, mabasi huwa yanapata shida kupita.

Je, ni nini kauli Serikali kuweza kuzikarabati stand hizo ili zikae kwenye standard?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nicodemas Maganga, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Maganga kwa namna anavyowasemea wananchi wa Mbogwe. Lakini nitoe maelekezo kwamba Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe afanye tathmini ya gharama zinazohitajika kufanya matengenezo kwenye stand hizi mbili ambazo ni chakavu sana ili tuone kupitia mapatao ya ndani wanaweza kufanya matengenezo, lakini kama mapato ya ndani hayatoshelezi basi waweze kuwasilisha maandiko ya kimkakati Serikali itafute fedha kwa ajili ya kutengeneza stand hizo. Ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Mji wa Kibara ndiyo makao makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda, lakini kwa bahati mbaya mpaka sasa hivi hatuna stand ya mabasi. Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusiana na suala hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Kajege kwa kazi nzuri na kubwa anayowafanyia wananchi wa Mwibara, lakini nimuelekeze Mkurugenzi na Halmashauri kwa ujumla kuainisha eneo hili kama ni eneo la kimkakati na kwamba ni mahitaji ya Halmashauri ili kuona uwezekano wa kupata stand katika eneo hilo.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; kwa kuwa stand nyingi inakuwa unaingia tu kwa kuwa huna la kufanya lakini hazina mwelekeo wa stand; kwa nini Serikali haiji na model stand kwa Makao Makuu ya Mikoa zikafanana zote kama vile ilivyo vituo vya polisi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asha Juma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze kwa kazi kubwa anayoifanya kuwasemea Watanzania kwa ujumla wake, lakini Serikali tulishatoa maelekezo na standard drawings za stand za ngazi ya Halmashauri, Mikoa lakini na majengo mengine. Kwa hiyo suala hili tunaendelea kuliboresha, kumekuwa na utofauti, kati ya mikoa na mikoa, lakini tumeshatoa sasa utaratibu ambayo ile michoro yote itakuwa inafanana. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuwa usafirishaji wa abiria ni jambo la muhimu kwenye nchi yoyote yenye ustaarabu.

Je, Serikali haioni ni muda sahihi sasa wa kuhakikisha wanatengeneza mkakati maalum wa kuzijenga stand kwenye miji inayoendelea ikiwemo Mlandizi ili kuachana na mipango ya mradi wa kimkakati ya Halmashauri isiyotekelezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Mwakamo, Mbunge wa Jimbo la Kibaha Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mwakamo kwa ambavyo anawakilisha ipasavyo wananchi wa Jimbo la Kibaha Vijijini, lakini Serikali ilishaweka mkakati tayari wa kujenga stand katika maeneo yote ambayo yanahitajika na ndiyo maana tunatekeleza kwa njia ya aina mbili; moja kwa mapato ya ndani ya Halmashauri kwa gharama zile ambazo zinafikika lakini kwa kutumia miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati tayari upo na tunaendelea kuutekeleza, suala ni Halmashauri pia kuhakikisha kwamba wanawasilisha mahitaji hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji.
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Spika, ahsante, stand ya Lindi Manispaa bado haiko vizuri, mabasi yote yanayotoka Mtwara, Songea na mkoa mzima kwa ujumla yanapitia pale.

Je, Serikali ina mkakati gani kujenga stand ile kuu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tecla Ungele, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Ungele amekuwa ni miongoni mwa Waheshimiwa Wabunge ambao wanawasemea sana wananchi kwa Watanzania kwa ujumla na wananchi wa Mkoa Lindi, naifahamu sana stand ya Manispaa ya Lindi kwa sababu nimekuwa kule kwa miaka kadhaa, ninafahamu kwamba tunahitaji kuijenga, tuotoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi, kutambua hii ni kipaumbele cha Halmashauri kufanya tathamini ya gharama na kuona kama inaweza ikajengwa kwa mapato ya ndani au wawasilishe kama mradi wa kimkakati. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Boma la Zahanati la Isusumia limemalizika tangu mwaka 2016. Naomba kujua ni lini sasa Serikali itatenga fedha ili boma lile liweze kumalizika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Wilaya ya Chemba kwa ujumla ina maeneo makubwa ya kilimo na hivyo kuna wahamiaji wengi sana. Nini mkakati wa Serikali wa kujenga zahanati kwenye maeneo yale sasa wamehamia watu wengi wa kutosha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na boma la Zahanati ya Lusubi ambayo limekamilika tangu mwaka 2016; nitoe maelekezo kwa Wakurugenzi wote wa Halmashauri za Wilaya kote nchini akiwepo Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba, majengo yote ya kutolea huduma za afya yakikamilika ni wajibu wao kufuatilia usajili wa zahanati zile, lakini kuweka vifaa tiba vya kuanzia ilia Zahanati zianze kutoa huduma wakati tunasubiri fedha Serikali Kuu kwa ajili ya kuanza kutoa huduma kwenye vituo hivyo kwa maana ya vifaa vya ziada vinavyohitajika.

Kwa hiyo zahanati hii, itafutiwe vifaatiba mapema iwezekanavyo kupitia mapato ya ndani, lakini pia isajiliwe ili ianze kutoa huduma mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na maeneo ya Chemba ambayo yana wananchi wengi, mkakati wa Serikali ni kuhakikisha tunaendelea kujenga zahanati na vituo vya afya kwa maeneo ya kimkakati. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge aainishe maeneo hayo ya kimkakati Serikali ifanye tathmini na kuona mpango wa utekelezaji. Ahsante.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, katika Kata ya Ihanda kuna Kijiji cha Shilanga na Seketu ambazo zina maboma ya zahanati ambayo yamekaa muda mrefu sana. Upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha maboma hayo yanakamilika ili wananchi waweze kupata huduma za afya katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga, Mbunge wa Jimbo la Vwawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze wananchi wa Jimbo la Vwawa kwa kutoa nguvu zao na kujenga maboma ya zahanati, lakini nimuhakikishie kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kipindi cha mwaka mmoja zaidi ya maboma 900 ya zahanati yaliyoanza ujenzi kwa nguvu za wananchi yamekamilishwa na zoezi hili ni endelevu. Katika mwaka ujao wa fedha tuna maboma 300 ya zahanati kwa ajili ya ukamilishaji. Kwa hiyo tutahakikisha pia katika ukamilishaji huo maboma haya ya Jimbo la Vwawa pia tunayapa fedha kwa ajili ya kuanza kukamilisha kwa awamu. Ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nami nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kama ilivyo Wilayani Chemba, Jimbo la Tabora Mjini lenye Kata 29 wananchi maeneo mbalimbali katika kata hizo wamejenga kwa kujitolea zahanati ambazo sehemu nyingi wamefikia kwenye maboma. Sasa je, ni lini Serikali itasaidia hizo juhudi za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Emmanuel Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, maboma haya ya zahanati ambayo yamejengwa na wananchi katika Jimbo la Tabora Mjini ni sehemu ya mkakati wa Serikali kuendelea kuyatambua kwa awamu na kuyatengea fedha kwa ajili ya kuyakamilisha. Ni sehemu ya bajeti ya maboma 300 katika mwaka ujao, tunajua hatuwezi kumaliza yote, lakini tutakwenda kwa awamu katika majimbo yote likiwepo Jimbo hili la Tabora Mjini. Ahsante.

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati ya Mwaiksabe majengo yake yamekuwa ni ya muda mrefu lakini pili walikuwa hawana jengo la mama na mtoto; wananchi wale wamejenga jengo la mama na mtoto na mpaka wamepaua.

Je, Serikali ni lini itawapelekea fedha kwa ajili ya kukamilisha hatua zilizobaki kwa maana ya plasta pamoja na vifaatiba? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze wananchi hawa katika zahanati hii kwa kutoa nguvu zao na kujenga jengo la mama na mtoto na hicho ni kipaumbele cha Serikali. Naomba nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri kufanya tathmini ya gharama zinazohitajika kukamilisha jengo hilo ili tuone kama wanaweza kutumia fedha za mapato ya ndani kukamilisha au Serikali Kuu. Lakini nikuhakikishie kwamba vifaatiba Serikali imetenga bilioni 69.9 mwaka ujao wa fedha tutapeleka pia katika jengo hilo. Ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Changamoto iliyopo katika Wilaya ya Chemba inafafana sawa na changamoto zilipo katika Jimbo la Mbinga Mjini. Kuna zahanati katika vijiji vya Mzopai, Mundeki, Mikolola, Maande na Rudisha nguvu za wananchi zimewekezwa pale. Kwa hiyo, nilitaka nijue ni lini Serikali itafanya mkakati kuhakikisha kwamba inakamilisha ujenzi wa zahanati ile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, majengo haya ya maboma ya zahanati katika Jimbo la Mbinga Mjini, kwanza tunawapongeza wananchi kwa kutoa nguvu zao kwa sababu huu ndiyo mpango wa maendeleo ya afya ya msingi kuchangia nguvu za wananchi katika ujenzi wa vituo hivi, lakini nimuhakikishie kama ambavyo Serikali imeendelea kukamilisha maboma katika mwaka huu zaidi ya maboma 900 ya zahanati na mwaka ujao 300; tutaendelea pia kutoa kipaumbele katika maboma haya ya Mbinga Mjini ili yaanze kukamilishwa kwa awamu. Ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Wananchi wa Isansa wamehamasisha kwa kutumia mapato ya ndani ya kituo cha afya wamechanga milioni 56 pamoja na matofali na mchanga; wameanza ujenzi wa wodi ya kinamama na wazazi katika kituo cha afya. Nini kauli ya Serikali katika kuwaunga mkono wananchi hawa Kata ya Insasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Jimbo la Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa Serikali ni kuendelea kukamilisha majengo ya zahanati na vituo vya afya, hospitali za halmashauri kwa awamu. Kwa hivyo, katika mipango hii tutaendelea pia kuhakikisha tunatambua maeneo haya ya Mbozi ili nayo yaweze kuingia kwenye bajeti kwa awamu kwa ajili ya ukamilishaji wake. Ahsante.

MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali; kwa kuwa Kituo cha Afya Mtina kinahudumia zaidi ya kata nne na changamoto ya kituo kile ni pamoja na kutokuwa na huduma ya upasuaji.

Je, Naibu Waziri anaweza kunihakikishia baada ya Bunge hili atembelee kituo kile ili aweze kuona changamoto za wananchi wa kata ile?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kwa kuwa Jimbo la Tunduru Kusini lina kata 15, vituo vya afya vinavyopatikana mpaka sasa ni vitatu ambavyo vyote havituoi huduma ya upasuaji kutokana na tatizo la kutokuwa na vifaa vya upasuaji, lakini kwa kuwa tunahitaji vituo vya afya vingi.

Je, Serikali ina mpango gani ya kuongeza angalau vituo vya afya viwili katika Kata ya Malumba na Kata ya Msechela ambazo zipo mpakani mwa Msumbuji ili kutoa huduma kwa wananchi wale ambao wanahudumiwa kutoka mbali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Jumbo la Tunduru Kusini kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mtina, Serikali imeshatenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji. Kwa hiyo, katika mwaka ujao wa fedha tuna uhakika sasa changamoto hiyo tutakuwa tumeondokana nayo, lakini nipo tayari kuambatana na Mheshimiwa Mpakate kwenda kutembelea kituo cha afya hiki na vituo vingine katika Jimbo lake ili kuona utoaji wa huduma lakini pia kuweka mipango ya pamoja kuhakikisha tunaboresha huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na ujenzi wa vituo vya afya katika kata zake 15 tunachukua kata zake mbili na bahati njema Waheshimiwa Wabunge walileta kata tatu za kipaumbele na Serikali inapitia huko kuandaa mpango wa utekelezaji wa ujenzi wa vituo vya afya kwenye kata tatu za kipaumbele kwa kila jimbo. Kwa hiyo, tutafanya hivyo katika jimbo hili la Tunduru Kusini. Ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Katika Jimbo la Kilwa Kaskazini Serikali ikishirikiana na taasisi ya Pan African ilijenga kituo cha afya katika Kata ya Somanga, lakini kituo kile kimekuwa na changamoto kubwa sana ya upatikanaji wa vifaatiba.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka vifaatiba ili huduma bora ya afya iweze kutolewa katika Kata ya Somanga?
NAIBU WA ZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais wetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametenga shilingi bilioni 69.95 mwaka ujao wa fedha kwaajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwenye vituo vya afya na hospitali za halmashauri. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge akiwemo Mheshimiwa Mbunge wa Kilwa Kaskazini kwamba kituo hiki cha afya ni miongoni mwa vituo ambavyo vitapelekewa vifaa tiba pamoja na vituo vingine vilivyokamilika ili viweze kuanza kutoa huduma za afya. Ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza nishukuru majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ambayo yanaonesha hali halisi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri 24 kati ya 184 ni chache sana na ni dhahiri kwamba kasi ni ndogo sana ya utekelezaji wa kifungu hiki cha sheria. Je, Serikali sasa imejipanga vipi kuhakikisha kwamba inaondoa vikwazo vyote ambavyo vinazuia utekelezaji mzuri wa sheria hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; suala la elimu ni muhimu sana katika kuhakikisha kwamba sheria hii inatekelezwa vizuri, lakini elimu hii inaonekana haijawafikia walengwa.

Je, Serikali ina mpango gani sasa wa kuhakikisha kwamba inatoa elimu kwa wale maafisa wanaohusika na manunuzi ya umma, lakini vilevile wale walengwa wa makundi maalum lakini hata zile taasisi ambazo zinahusika...

SPIKA: Mheshimiwa Anastazia Wambura umeshauliza mawili au hilo la mwisho lile lina vipengele?

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, sijauliza mimi natoa tu, ni swali la pili hili, la kwanza nimeuliza.

SPIKA: La kwanza nimekusikia.

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ndiyo.

SPIKA: Ndiyo hilo la pili naona kama lina vipengele hivi?

MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, hapana ni kwamba elimu itolewe kwa yale makundi yanayohusika na utekelezaji wa hii sheria na makundi yenyewe ni yale makundi maalum, lakini pia wale maafisa wanaohusika na manunuzi, lakini pia taasisi zinazosimamia yale makundi maalum. Ndiyo nataka sheria hii itolewe elimu yake kwa makundi haya matatu, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anastazia Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kasi ya vikundi hivi kunufaika na mpango huu wa asilimia 30 bado ni ndogo. Halmashauri 24 kati ya 184 bado kasi ni ndogo na ndiyo maana Serikali imeweka utaratibu wa kuonesha kwamba tunahamasisha vikundi kuhakikisha wananufaika na asilimia 30 kupitia Maafisa Maendeleo ya Jamii kuhamasisha vikundi hivyo, lakini pia kuto elimu ili waweze kujisajili PPRA.

Mheshimiwa Spika, nani kuhusiana na mpango huo tutaendelea kuhakikisha kwamba tunawaelekeza Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa zote kote nchini kuhakikisha kigezo hicho kinazingatiwa kwenye bajeti. Kwanza kutenga asilimia 30 ya fedha zote za ununuzi pili kuhamasisha vikundi vyenye sifa hiyo na kuviwezesha kusajiliwa PPRA. Ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY J. MAKOA: Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba nimeuliza swali ni lini, nilitegemea ningeambiwa mwezi ujao maana yake imekuwa ni story ya muda mrefu; nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, je, vituo vya afya vilivyopo Kata ya Suruke, Kingale pamoja na sasa tunajenga Kolo vitakuwa miongoni mwa orodha ya mgao huo?

Mheshimiwa Spika, la pili; kumekuwa na hofu kubwa kwa wananchi wa Kondoa wanaopata huduma katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji hasa wanapopata kesi ya kufanyiwa operation, sasa pamoja na ahadi hiyo ya kupatiwa ambulance wamekuwa wakipata rufaa kwa tabu sana kuletwa Hospitali ya Mkoa lakini hata hivyo, wananchi wamekuwa na mashaka makubwa.

Je, Serikali itakuwa tayari lini kwenda kujiridhisha na uwezo wa madaktari pamoja na vifaatiba vilivyopo katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Jimbo la Kondoa Mjini, kama ifuatayo: -

Mheshimiwa Spika, fedha ambazo zinakwenda kununua magari haya ya wagonjwa 195 ambazo zinatoka kwenye mpango wa UVIKO-19 zitakwenda kununua magari haya na yatapelekwa kwenye Halmashauri zote 184 lakini ni maamuzi ya halmashauri kuona uhitaji mkubwa katika ngazi ya hospitali au katika kituo cha afya ambako gari litapelekwa. Kwa hiyo, ni maamuzi ya halmashauri kuona kipaumbele kwa wakati huo gari hilo litakwenda kwenye kituo cha afya au kwenye hospitali ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu tunapanga kununua magari haya na UNICEF kuna uwezekano mkubwa magari ya wagonjwa yakaongezeka zaidi ya 195. Kwa hiyo, tunauhakika vituo vyetu pia ambavyo vimekamilika vitapata magari ya wagonjwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na uhakika wa huduma katika Hospitali ya Mji wa Kondoa kwa maana ya uwezo wa madaktari na vifaatiba; madaktari wote wanaoajiriwa kwa ngazi zao wanakuwa wamesajiliwa na Serikali imejiridhisha juu ya uwezo wao wa kutoa huduma. Kwa hiyo, niwatoe hofu wananchi wa Mji wa Kondoa kwamba madaktari waliopo pale ambao wamepelekwa na Serikali wana uwezo unaotakiwa, wanatoa huduma ambazo zinatakiwa, lakini kama kuna mapungufu Serikali tutafuatilia na kuchukua hatua katika maeneo hayo. Ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Katika Jimbo la Kilwa Kaskazini lenye hospitali moja na vituo vya afya vitatu kumekuwa na changamoto kubwa ya uwepo wa gari la wagonjwa. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka magari ya wagonjwa ya kutosha ili kutoa huduma kwa wagonjwa wa dharura? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kati ya magari hayo 195 plus Halmashauri ya Kilwa ni miongoni mwa halmashauri ambazo zitapata magari hayo na tutafanya tathimini kuangalia umbali wa vituo hivi lakini na idadi ya wananchi wanao hudumiwa ili ikiwezekana tuongeze magari kwenye Wilaya hiyo ya Kilwa. Ahsante.

MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, nashukuru, Halmashauri ya Kinondoni ina majimbo mawili; Jimbo la Kinondoni na Jimbo la Kawe lakini Jimbo la Kawe tumejenga hospitali kubwa sana ambayo itatumika na Bagamoyo na Kawe, lakini vilevile referral’s zinaweza zikaenda Mloganzila. Sasa kutokana na ukubwa na upekee wa hospitali ya Kawe iliyokuwa Mabwepande hamzani kwamba Jimbo la Kawe linatakiwa lipate gari kwa upekee? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima James Mdee, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunafahamu hospitali kubwa ya Mabwepande katika Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni imejengwa, imekamilika itaanza kutoa huduma wakati wowote hivi sasa tumeanza na huduma za OPD na ni lazima tutapeleka gari la wagonjwa pale kulingana na ukubwa wa hospitali ile na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kawe pia amekuwa akikumbushia sana kuhusiana na umuhimu wa gari hilo. (Kicheko)

Kwa hiyo, nikupongeze sana Mheshimiwa Mdee kwa kushirikiana sana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Kawe, ahsante.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi; pale kwenye Kata ya Tandale Jimbo la Kinondoni kuna kituo cha afya ambacho kinahudumia zaidi ya watu 1,000 kwa siku na Mheshimiwa Naibu Waziri anafahamu, lakini kituo kile hakina gari la wagonjwa nafahamu mtaleta magari hayo ambayo mmeyataja lakini kwa Kinondoni mahitaji ni makubwa.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuipelekea gari kituo cha Afya cha Tandale ili kuweza kuondoa matatizo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abbas Tarimba, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimejibu kwenye majibu yangu ya msingi tunakwenda kununua magari 195 lakini tutaongeza magari mengine kwa sababu kwa utaratibu ambao tunanunua magari haya kupitia UNICEF tutapata saving ambayo tuna uhakika magari yataongezeka na kigezo cha kugawa magari haya itakuwa ni vitu vyenye idadi kubwa ya wagonjwa kama Tandale na maeneo mengine, lakini umbali kutoka kituo kile kwenda hospitali ya halmashauri.

Kwa hiyo, nimhakikishiwa Mheshimiwa Mbunge tutafanya tathimini ya uhitaji huo na pale ambapo vigezo vitafikiwa tutaleta gari pia katika vituo hivyo. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi pamoja na mpango mzuri wa Serikali kupeleka magari ya wagonjwa kila halmashauri.

SPIKA: Taja kituo cha afya ama hospitali na uliza swali lako.

MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, na kwa kuwa Wilaya ya Hanang kuna upande wa juu ambapo kuna kata nane na tumejenga vituo viwili vya afya vya Basutu na Hirbadaw, je, Serikali ipo tayari kutuletea gari la pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Hhyuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang kama ifuatavyo; nimhakikishie kwamba tufanya tathimini na kuona uhitaji wa magari katika vituo hivyo na tutapeleka kadri ya upatikanaji wa magari hayo. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa na mimi nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu inajumla ya vituo vya afya nane lakini vituo vitatu tu ambavyo vinamagari haya ambulance na jiografia ya wilaya yangu ni ngumu kweli kweli. Nilikuwa nataka niombe pamoja na mpango wa wizara kuhakikisha kwamba inatoa..

SPIKA: Mheshimiwa Butondo uliza swali unataka gari iletwe/ipelekwe wapi?

MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, ninaomba kuletewa gari na lipelekwe katika Tarafa ya Mondo ambayo itaongeza uwepo wa magari katika Tarafa hiyo.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Boniphace Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimuhakikishie kwamba katika tathimini ambayo tutafanya kubaini uhitaji wa magari ya wagonjwa na vigezo kama vinafikiwa tutafanya pia katika vituo vya afya ya Kishapu ili tuweze kufanya maamuzi hayo, ahsante.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona; Hospitali ya Rufaa ya Kitete ina changamoto kubwa sana ya magari ya kupebea wagonjwa. Je, katika magari hayo 195 hospitali hii ipo katika list?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Hawa Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, magari haya 195 ni magari ambayo yatanunuliwa na Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya vituo vya huduma za afya za msingi kwa maana zahanati, vituo vya afya na hospitali za halmashauri, lakini nikuhakikishie kwamba kupitia Wizara ya Afya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametenga fedha kununua magari mengi kwa ajili ya wagonjwa kwenye hospitali za rufaa za mikoa kanda na hospitali ya Taifa. Kwa hiyo hospitali ya Kitete ni sehemu ya wizara ya afya na magari hayo pia yapo kwa ajili ya hospitali hiyo kupitia wizaza ya afya, ahsante.
MHE. KILUMBE S. NG'ENDA: Mheshimiwa Spika, mimi najua nimo katika mgao wa magari, lakini nilichotaka kujua kwa sababu Wabunge tumekuwa tukipigia kelele sana suala hili la magari. Je, ofisi yako itaandaa utaratibu ili kila Mbunge apokee gari hii kwenye eneo lake? (Makofi/Kicheko)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Kirumbe Ng’enda, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, magari haya yanakwenda kwenye Halmashauri zetu ambako sisi Waheshimiwa Wabunge tunatoka huko, tunatambua kuna halmashauri zenye jimbo zaidi ya moja, consideration itafanyika kuona idadi ya vituo katika jimbo husika lakini pia uhitaji wa magari ya wagonjwa na tutapeleka hivyo. Ahsante.

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo cha Afya Igulubi kilichopo kwenye Jimbo la Igunga kimejengwa kwa milioni 500 na Serikali ya Chama cha Mapinduzi na kituo kipya hakina gari la wagonjwa. Je, nini kauli ya Serikali kuhusu hilo? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Nicholaus Ngassa, Mbunge wa Jimbo la Igunga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kituo hiki cha afya ambacho kimekamilika ni sehemu ya vituo ambavyo vinahitaji magari ya wagonjwa, lakini safari ni hatua tutafanya tathimini kuona vigezo hivyo na kama itatimiza vigezo basi itapata gari la wagonjwa.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, kituo cha afya cha Matembanga kiko kilometa 80 kutoka hospitali ya Wilaya ya Tunduru Mjini na tayari tunaishukuru Serikali majengo ya upasuaji yamekamilika na vifaa vyote vimekamilika na tumeanza upasuaji hapa majizi na kituo kile hakina gari la wagonjwa.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupatia gari la wagonjwa kituo kile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Kungu, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba tunafanya tathimini ya vituo vya afya ambavyo vimekamilika na vinatoa huduma za upasuaji kikiwemo kituo hiki na kuona uwezekano wa kupata gari la wagonjwa, lakini itategemea idadi ya magari ambayo tunayo na kipaumbele cha halmashauri kulingana na vigezo vya kitaalamu vya uhitaji wa magari ya wagonjwa.

MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa zahanati ya Town Clinic ya Tabora Manispaa ambayo Naibu Waziri anaifahamu vizuri ina wagonjwa wengi na haina gari la wagonjwa; ni lini sasa Serikali itatuletea gari la wagonjwa kwa ajili ya kusaidia kata hizo 30 ambazo inaitumia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Munde Abdallah, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba zahanati hii inahudumia wananchi wengi, lakini kigezo cha gari ya gari la wagonjwa ni kuwa kituo cha afya au hospitali ya halmashauri, lakini kwa sababu ya upekee wa zahanati hii tutafanya tathimini na kuona uwezekano wa kupeleka gari baada ya kujiridhisha na vigezo ambavyo vinatakiwa, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa kituo cha afya cha Kata ya Mkuyuni kinachangamoto ya gari la wagonjwa; je, na sisi lini tutaletewa gari la wagonjwa?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamisi Taletale, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, magari haya yatakayo kuja yatapelekwa kwenye vituo vyetu vikiwemo vya Morogoro ambavyo vitakidhi vigezo. Kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutawasiliana tuone namna ya kufanya tathimini kwenye kituo hiki kama kinakidhi vigezo hivyo, ahsante.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, ahsante; ni lini Serikali itakuwa tayari kupeleka gari la wagonjwa Kituo cha Afya Bulale kulingana na Geografia yake ilivyo mbali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Stanslaus Mabula, Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bulale nakifahamu tulishafanya ziara pale, kiko mbali na kinahudumiwa wananchi wengi naomba Mheshimiwa Mbunge shirikiana na halmashauri kuweka kipaumbele cha kituo au hospitali ambayo tunahitaji kupata gari ili ikipatikana tupeleke hapo, lakini baadaye tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka magari katika kituo hicho pia.

MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante nashukuru na ninashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali kweli Waziri amekuwa akinipa ushirikiano sana.

Lakini nilitaka nijue sasa ni lini mtaalam huyo ataletwa kwa sababu tatizo hili limekuwa ni la muda mrefu sana leo Wilaya ya Meatu hospitali ina zaidi ya miaka 30 lakini hatujawahi kupata mtaalam wa kudumu wa X-ray, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Minza amekuwa akifuatilia sana sana kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Meatu kupata mtumishi kwa ajili ya huduma za X-ray kwenye hospitali ya Meatu na nimuhakikishie kwamba katika ajira hizi ambazo tunakamilisha na mpango ni kuanzia Julai watumishi wetu watapelekwa vituoni tutapeleka mtaalam wa X-ray kwenye hospitali hii ya Meatu, ahsante. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, mwezi Oktoba mwaka jana Mheshimiwa Waziri Mkuu alitembelea katika Jimbo la Kilwa Kaskazini na alifika katika hospitali ya Kipatimu na akakuta kuna changamoto kubwa ya mtumishi wa X-ray baada ya kuwa X-ray ilinunuliwa miaka zaidi ya minne kabla ya mwaka jana ikiwa haitumiki kutokana na kukosa mtumishi wa X-ray.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni kwamba mtumishi huyu aliletwa akakaa miezi sita lakini juzi juzi hapa ameondolewa, nataka kujua je, Serikali ina mpango gani wa kumrejesha yule mtumishi ambaye ameondolewa juzi juzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tulipeleka mtumishi Hospitali ya Kipatimu lakini kwa sababu za kiutumishi amehamishwa, lakini kwenye ajira hizi ambazo watumishi watapelekwa mwezi Julai tayari ameshapangwa mtumishi wa X-ray kwenye Hospitali ya Kipatimu, ahsante.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Pamoja na uhaba wa watumishi/wataalam wa hivyo vifaa tiba lakini pia ma-engineer au mafundi wa kutengeneza hivyo vifaa tiba pindi inapoharibika inakuwa ni changamoto kubwa sana.

Je, katika ajira zilizoko mnazingatia pia na wataalam hawa ili inapopata breakdown yoyote basi inatengenezwa kwa wakati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Ni kweli kwamba tumekuwa na changamoto ya upungufu wa wataalam wa vipimo kwa maana diagnostic issues ikiwemo X-ray na ultrasound, lakini Serikali kwanza tumeweka mpango mkakati wa kuwafanyia mafunzo kazini wataalam zaidi ya 300 ambao watakwenda ku-cover mapengo kwenye vituo vya afya na hospitali ambazo zinajengwa ili yale majengo yaliyojengwa na vifaa tiba ambavyo vinakwenda vianze kutumika mapema iwezekanavyo.

Lakini pili tuna wataalam wa ufundi kwa maana ya biomedical engineers katika halmashauri zetu na katika ajira hizi pia wataajiri wataalam hao, ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, vituo vya afya vya Kasaunga, Kisorya na Kasuguti bado havina mashine za X-ray; je, ni lini vituo hivi vitapata hizo mashine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kupitia mpango wa UVIKO-19 Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa fedha kwa ajilli ya kununua digital X-ray 65 kwa ajili ya halmashauri zetu, lakini kwa sababu tunakwenda kununua kwa utaratibu wa kushirikiana na wenzetu wa UNICEF zinaweza zikafika zaidi ya 80, 90.

Kwa hiyo vituo vingi vile ambavyo vinahitaji X-ray vitapata, lakini kwa maana ya hospitali za wilaya kama kipaumbele na baadaye tutakuja kwenye vituo hivyo na tuta-consider pia vituo vya Mwibara, ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Spika, na mimi nina swali la nyongeza; hospitali ya halmashauri ya Mji wa Mbulu X-ray machine mbovu, kwa hiyo kufanya watu hawa kuhangaika kwenda kwenye vituo vya afya. Je, Serikali inapeleka lini X-ray machine katika Hospitali ya Mji wa Mbulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yustina, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika X-ray ambazo zitaletwa kipaumbele ni hospitali za halmashauri, kwa hiyo tunachukua hoja ya hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbulu ili tuone kama ile X-ray haiwezi kufanyakazi basi tuhakikishe katika awamu hii tunapeleka X-ray pale wananchi wapate huduma, ahsante.
MHE. DKT. MATHAYO D. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza kwa Jimbo la Same Magharibi.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Hedaru na Kituo cha Afya cha Kisiwani, ni vituo ambavyo vinahudumia watu wengi sana lakini vina upungufu wa vifaa tiba. Je, ni lini Serikali itahakikisha kwamba Kituo cha Afya Hedaru na kile cha Kisiwani kinapata vifaa tiba vya kutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Mathayo David Mathayo, Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi kama ifuatavyo: -

Katika bajeti ya mwaka ujao wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya kununua vifaa tiba kwenye hospitali za halmashauri zilizokamilika na vituo vya afya vilivyokamilika vya awamu ya kwanza.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kama vituo hivi vipo awamu ya kwanza nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vitapata vifaa tiba lakini kama viko awamu ya pili na ya tatu basi vitapata awamu itakayofuata, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Hospitali ya Makambako imeshapata X-ray na Ultrasound naomba kuuliza swali moja tu la nyongeza; Kituo cha Afya Ikizu kina muda mrefu sana tukiwa na maombi ya X-ray na mwaka jana walisema wangepata lakini hawajapata. Ni lini sasa Kituo cha Afya Ikizu kitapata X-ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vyetu vya afya vingi havina mashine za X-ray, lakini bado tutaangalia vigezo ambavyo vitapelekea baadhi ya vituo kupata kipaumbele kuliko vituo vingine, kwa hiyo, naomba nichukue hiki Kituo cha Afya cha Ikizu ili tukafanye upembuzi na kuona uhitaji wa X-ray lakini baada ya hapo tutatafuta X-ray kwa ajili ya kituo hicho pia, ahsante.
MHE. DUNSTAN L. KITANDULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Kituo cha Afya cha Maramba kinachohudumia kata sita Serikali iliahidi kupeleka X-ray; ni lini Serikali itapeleka X-ray?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dunstan Kitandula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Maramba ni kweli kwamba kinahudumia kata nyingi na katika mpango ambao tumeuweka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kituo hiki pia ni miongoni mwa vituo ambavyo tumepanga kitapelekewa X-ray, ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja na nasema ni ombi; kwanza nachukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa kazi nzuri sana ambayo inafanyika katika jimbo langu. Naomba Mheshimiwa Waziri anihakikishie kwamba baada ya Bunge hili tutaongozana naye tuweze kwenda Mwibara ili tukatembelee shule za msingi na zahanati husika.
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Charles Muguta Kajenge, Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Mheshimiwa Kajege kwa kazi kubwa anayofanya kuhakikisha wananchi wa Jimbo la Mwibara lakini tupokee shukrani nyingi na pongezi zake kwa Serikali yetu inayoongozwa na Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na nimuhakikishie kwamba tutaendelea kutekeleza miradi hii kwa mnufaa ya wananchi wa Mwibara, lakini nikuhakikishie kwamba niko tayari tuambatane pamoja baada ya Bunge hili kwenda Mwibara kupita vituo, lakini pia na miradi mingine ya Serikali. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi; kwa kuwa Serikali imeamasisha wananchi kujenga zahanati katika kila kata na vijiji na maboma mengi hayajakamilika, je, nini kauli ya Serikali kukamilisha maboma hayo katika Halmashauri ya Shinyanga?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali ilihamasisha wananchi kwa nia njema ya kuhakikisha kwamba wananchi wanapata zahanati na vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati na mpango wa Serikali ni kukamilisha zahanati na maboma ya vituo hivyo katika maeneo ya kimkakati kwa maana ya kata za kimakakati na tarafa za kimkakati, siyo kila kata au siyo kila kijiji na kazi hiyo imefanyika sana kwa mfano katika mwaka mmoja maboma ya zahanati 954 yamekamilishwa, mwaka ujao Serikali imetenga bilioni 15 kwa ajili ya kukamilisha maboma 300 ya zahanati, kwa hivyo kazi hii itaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Kwa vile Serikali ilishaahidi kutoa bilioni moja kuanzia Julai na tunaamini itakuja; je, sasa Manispaa ya Bukoba Mjini ianze kutangaza tender kama TARURA wanavyofanya?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili kwa kuwa stendi ya Bukoba Mjini imewekwa katika miradi ya TACTIC, naomba kujua utekelezaji wa mradi huu utaanza lini katika Manispaa ya Bukoba?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana Semuguruka kwa namna ambavyo anashirikiana kwa karibu sana na Mheshimiwa Mbunge Stephen Byabato, Mbunge wa Bukoba Mjini kuhakikisha miradi inakwenda vizuri, lakini nimuhakikishie kwamba suala la ahadi ya Serikali ya bilioni moja ni ahadi ya Serikali na tutahakikisha fedha hiyo inakwenda mwaka wa fedha ujao tunaoanza Julai ili kazi zianze. Lakini ni vema tusubiri fedha ziingie ndipo tuanze kutangaza zabuni kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kuhusiana mradi wa TACTIC unaoanza awamu ya pili mwaka wa fedha baada ya 2022/2023. Ahsante.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza.

Kwa kuwa Mkoa wetu wa Iringa kuna stendi ile ya Igumbilo tunashukuru, lakini stendi ile iko mbali sana na wananchi imekuwa ni mateso wananchi wamekuwa wakifika usiku sana wanapigwa na wajambazi.

Je, hivi ni kanuni au sheria kwamba haya mabasi yasishushe abiria katika stendii za zamani kwa sababu wananchi wengi wengi wanapata mateso makubwa sana?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali siku zote ni kuboresha huduma za wananchi, lakini pia kurahisisha Maisha ya wananchi katika maeneo yao. Kwa hiyo naagiza Mkuu wa Mkoa wa Iringa lakini na menejimenti nzima ya Mkoa wa Iringa kufanya tathimini ya athari ambazo zinatokana na kuacha kutumia stendi ya zamani na kutumia stendi mpya peke yake na kuona busara inaongoza nini ili wananchi wapunguziwe adha ya usafiri. Ahsante sana.

MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais alipopita Lamadi Wilaya ya Busega aliahidi ujenzi wa stendi, je, ni lini utaanza ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahadi za viongozi wetu ni maelekezo kwa Wizara na mimi nimhakikishie kwamba tumeshapokea maelekezo hayo tunachofanya sasa tunatafuta fedha, lakini tunafanya usanifu kwa ajili ya kutafuta fedha, lakini tunafanya usanifu kwa ajili ya kuanza kujenga stendi ya mabasi ya Busega baada ya kupata fedha kwa ajili ya shughuli hiyo. Ahsante sana.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Njombe stendi ya Mkoa iko Njombe na kwa sababu Njombe ni pembezoni mwa mji, unapozungumzia mji ni Makambako ambako ndiyo highway ya kwenda Malawi kwenda Songea, kwenda Mbeya na kadhalika. Ni lini sasa stendi ya mabasi ya Mji wa Makambako itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga almaarufu Jah People, Mwenyekiti wetu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, stendi ya Mkoa wa Njombe ni kweli iko katika mji wa Njombe, lakini naomba tukubaliane kwamba tunaichukua hoja hii ya Mheshimiwa Deo Sanga, nafahamu Makambako pale tuna stendi, lakini ni stendi ya mji inayohitaji maboresho kwa hiyo tutakaa mimi na Mheshimiwa Sanga tukubaliane tuone Wizara inaweza ikafanya nini kuboresha stendi pale Makambako Mjini. Ahsante.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kuweza kuniona.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Mbea ni miongoni mwa majiji makubwa katika nchi yetu ya Tanzania, lakini mapka sasa hatuna stendi yenye hadhi ya jiji.

Je, ni lini sasa Serikali itajenga stendi yenye hadhi ya jiji kwenye mkoa wetu wa Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kasaka, Mbunge wa Jimbo la Lupa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Jiji la Mbeya ni jiji kubwa, lakini bado tunachangamoto ya stendi inayofanana na hadhi ya Jiji la Mbeya, lakini nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Tulia Ackson, Mbunge wa Mbeya Mjini pia amekuwa akifuatilia sana suala hilo nakushukuru sana kwa kumuunga mkono, lakini Serikali inafanya tathimini na tumeshaelekeza Halmashauri ya Jiji la Mbeya kuleta andiko la mapendekezo ya kujenga stendi ili tuone kama wanaweza kujenga kwa mapato ya ndani au kama mradi wa kimkakati ili Serikali tutafute fedha kwa ajili ya ujenzi huo. Ahsante.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali ina mpango gani wa kujenga stendi ya mikoani katika Jimbo la Mbagala hasa Mikoa ya Kusini?

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abdallah Chaurembo, Mbunge wa Mbagala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Mbagala ni eneo ambalo wananchi wengi wa Mikoa ya Kusini wanatumia kama sehemu ya kufikia au kuanza safari kuelekea mikoa ya Kusini, kwa hiyo nimuombe Mheshimiwa Mbunge lakini niagize Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kufanya tathimini ya uwezekano wa kutekeleza mradi huu kwa maana ya kupata eneo, lakini pia kufanya makadirio ya gharama ili tuweze kuona kama Serikali nini kinaweza kikafanyika. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa kuwa Mji wa Namtumbo ni mji ambao unapita mabasi yanayokwenda Masasi, Mtwara, Lindi mpaka Dar es Salaam kwenda kwenye Kituo cha Mbagala, lakini hatuna stendi ya mabasi na halmashauri yetu haina uwezo wa kujenga stendi ya mabasi lakini uwanja upo. Je, Serikali ipo tayari kututengea fedha kujenga stendi ya mabasi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Jimbo na Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nitoe maelezo ya ujumla kwa wakurugenzi wote wa Mamlaka ya Serikali za Mitaa walishapewa maelekezo kuainisha vipaumbele vya miradi yenye tija kwa jamii zikiwemo stendi, kwa hiyo ni hoja ya msingi kwamba Wakurugenzi akiwepo Mkurugenzi wa Namtumbo walete makadirio ya ujenzi wa stendi hiyo ili Serikali ione namna gani inaweza ikatekeleza mradi huo. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, Wilaya ya Lushoto hasa Lushoto Mjini stendi yake ni yazamani sana. Je, Serikali inampango gani wa kujenga stendi mpya sasa Wilayani Lushoto?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe halmashauri ya Lushoto na Mheshimiwa Mbunge kushirikiana nao kama sehemu ya Baraza la Madiwani kutuletea mapendekezo yao, lakini na tathimini ya gharama ili sasa Serikali iweze kuona utaratibu ambao utatumika kujenga stendi hiyo kwa sababu ni mahitaji ya wananchi. Ahsante.

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona; je, nini kinakwamisha ujenzi wa stendi mpya eneo la Madira kule Jimbo Arumeru Mashariki ambao mradi huu ulisitishwa katika hatua za mwisho katika utekeleza mwaka 2019?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ndiyo nimepata taarifa hii kwamba huo mradi umekwama naomba nilichukue hili baada ya session hii ya maswali na majibu nikae na Mheshimiwa Dkt. Pallangyo tujuwe hiyo stendi kwa nini imekwama na sisi tutatumia wataalamu wa Wizara kufanya tathimini lakini kukwamua mkwamo ambao hupo katika stendi hiyo. Ahsante.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza vituo hivi vitatu vya Bungu, Magoma na Mombo ni vituo vya muda mrefu na vinahudumia eneo kubwa; ni lini sasa hiyo tathmini inafayofanya na Serikali itakamilika ili Serikali ipate nafasi ya kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya maboresho?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, vituo hivi nilivyovitaja karibu kila kituo kimoja kinahudumia tarafa nzima, kata zaidi ya tisa. Zipo kata ambazo tumeziainisha kwa ajili ya vituo vya kimkakati; ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya vituo vya mkakati kwenye Jimbo la Korogwe Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba vituo hivi vya afya vitatu ni vituo vya siku nyingi na Serikali tayari tulishapeleka wataalamu kufanya tathmini ili kuona majengo yanayohitajika, lakini na gharama ambazo zinazohitajika. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakamilisha mapema iwezekanavyo ili Serikali iweze kutafuta fedha kwa ajili ya kwenda kuongeza majengo yanayopungua katika vituo hivi.

Mheshimiwa Spika, lakini kuhusu na vituo vya afya vya kimkakati, Serikali imeshaainisha maeneo yote nchini kote ambayo yanahitaji vituo vya afya vya kimkakati ikiwemo kwenye Jimbo la Korogwe Vijijini na fedha zinatafutwa kwa ajili ya ujenzi kwa hatua kadri ya upatikano wa fedha, ahsante sana.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi na mimi kuuliza swali dogo la nyongeza.

Katika Jimbo la Njombe Mjini kumekuwa na ahadi ya muda mrefu ya kupanua Kituo cha Afya cha Njombe Mjini kwa sababu hakina wodi za wanaume. Ni lini sasa Serikali itatekeleza ahadi hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deodatus Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Njombe Mjini ni moja ya vituo ambavyo Serikali tayari imeanza kufanya tathmini ya majengo ambayo yatahitajika ili utanuzi uweze kufanyika na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kazi hiyo itafanyika na tunatafuta fedha kwa ajili ya kupanua Kituo cha Afya cha Njombe.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika imejenga kwa mapato yake ya ndani kituo cha afya chenye hadhi ya hospitali eneo la Kalema, Kata ya Ikola, kituo hicho kimekamilika, tatizo lililopo ni ukosefu wa wataalamu na vifaa tiba.

Je, ni lini Serikali itawaunga mkono kwa kuwapelekea vifaa tiba na wataalamu ili kile kituo kianze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze sana halmashauri hii kwa kujenga kituo cha afya kwa mapato ya ndani, lakini nimwakikishie kwamba katika ajira ambazo zinaendelea hivi sasa ambazo kufikapo Julai Mosi watumishi watapelekwa katika vituo vyetu tutahakikisha kituo hiki pia kinapelekewa watumishi ili kianze kutoa huduma. Lakini katika mwaka ujao wa fedha tumetenga shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba ambavyo vitapelekwa ili kituo hiki kiendelee kutoa huduma za afya, ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, naomba kufahamu ni lini Serikali itatuboreshea Kituo cha Afya cha Isasa kwa maana ya kutujengea wodi ya akina mama pamoja na wodi ya akina baba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Juliana Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuainisha vituo vyote ambavyo vina majengo pungufu ili kuyajenga kwa awamu. Kwa hiyo, naomba nichukue hoja ya Mheshimiwa Juliana Shonza ili tuweze kuona majengo yapi yanapungua, gharama kiasi gani inahitajika ili tuanze kujenga majengo yanayopungua, ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, Kituo cha Afya Msandamuungano ni kati ya vituo vya afya vilivyoko ndani ya Jimbo la Kwela na kina miundombinu chakavu kimekuwa cha muda mrefu; je, Serikali mna mpango gani wa kuboresha hiki kituo cha afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deo Sangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumefanya tathmini ya vituo vyote kote nchini, vituo chakavu, hospitali chakavu ambazo zitapangiwa bajeti kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Tumeanza na hospitali za halmashauri, lakini tutakwenda na vituo vya afya ili kuvikarabati au kuviongezea majengo. Kwa hiyo naomba nichukue hoja yako Mheshimiwa Sangu ili tufanye tathmini pia katika kituo hicho na kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati na kuongeza majengo ya maeneo hayo, ahsante sana.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, Kata ya Kitanga iko kilometa 77 kutoka yalipo makao makuu ya Wilaya. Je, ni lini Serikali itajenga kituo cha afya katika kata hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kigezo kimojawapo cha kujenga vituo vya afya ni umbali wa eneo hilo husika kutoka kituo cha afya au hospitali ya karibu. Kwa hiyo kwa kilometa 77 bila shaka tunahitaji kuwa na kituo cha afya. Niagize Mkurugenzi wa Halmashauri hii kuhakikisha wanafanya tathmini ya kutafuta eneo, lakini pia watuletee maombi hayo kwa ajili kujenga kituo cha afya katika eneo hilo, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, asante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itaboresha na kupanua Kituo cha Afya cha Mvomero? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye mpango mkakati wa kupanua na kuboresha vituo vya afya tutahakikisha pia tunakifanyia tathmini kituo hicho na kutenga fedha ili tuende kukarabati na kupanua kituoo hicho kwa awamu, ahsante.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Napenda kuiuliza Serikali je, ni lini Serikali itaanza kujenga vituo vya afya katika kata za kimkakati za Kibata, Kandawale na Miguruwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha peke yake Serikali imeendelea kujenga vituo vya afya katika maeneo ya kimkakati na mpaka Juni hii tayari tumeshajenga vituo vya afya 234 nchini kote na mpango huu ni endelevu, tutahakikisha tunaendelea kujenga vituo vya afya ikiwemo katika Jimbo la Kilwa Kaskazini, ahsante.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ilemela, Kata ya Buswelu walijenga hospitali. Baada ya ukaguzi ikaonekana maeneo yale ni madogo ikahamishiwa Kata ya Sangabuya kwa ahadi kwamba maeneo yale yatakuja kupewa kituo cha afya. Lakini leo ni zaidi ya miaka minne hayajawa kituo cha afya.

Je, ni lini Serikali itaweka kituo cha afya katika majengo yale yaliyoko Kata ya Buswelu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwezi uliopita nilitembelea eneo hili la Kata ya Ilemela eneo la Buswelu na kuona yale majengo ambayo yamejengwa na Wizara ya Afya, lakini na jengo moja ambalo lilijengwa kwa ajili ya kituo cha afya, na nilitoa maelekezo majengo yale ifikapo mwisho wa mwaka ujao wa fedha yaanze kutoa huduma kama kituo cha afya badala ya kubaki bila kutoa huduma. Kwa hiyo, tumeshalifanyia kazi hilo na nimwakikishie kwamba litakwenda kukamilika, ahsante.
MHE. ERIC J. SHIGONGO: Mheshimiwa Spika, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri. Zangu ni shukrani kwa sababu Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo kituo hiki kijengwe baada ya mama mmoja kufia kwenye mtumbwi. Sasa nina swali moja tu la nyongeza.

Je, Serikali iko tayari kuifikiria Kata ya Bukokwa ambayo ina sifa zile zile kama Kisiwa cha Maisome ili iweze kupata kituo cha afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Eric James Shigongo, Mbunge wa Jimbo la Buchoswa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nipokee shukrani zake nyingi sana kwa Serikali ya Awamu ya Sita na Mheshimiwa Rais wetu kwa kazi kubwa anayoifanya katika Jimbo la Buchosa na nchini kote kwa ujumla, na nimwakikishie tu kwamba kata hii ambayo ameisema ameshakuja kufatilia mara nyingi kuhusiana na uhitaji wa kituo cha afya na tayari tumeanza kufanya tathmini kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya, ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Mufindi kwa ujumla makao yake makuu iko kwenye Kata ya Mtwango, lakini eneo hilo mpaka sasa pamoja na kwamba imehamishiwa makao makuu Mafinga Kata ya Mtwango yenye population kubwa haina kituo cha afya; je, ni lini Serikali sasa itapeleka kituo cha afya pale kwa ajili kuhudumia kata hiyo na kata jirani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa David Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kata hii ya Mtwango ni kata kubwa na ina wananchi wengi na Mheshimiwa Mbunge ameisemea mara nyingi na tumekubaliana tunatafuta fedha kwenda kujenga kituo cha afya katika kata hiyo, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi; Kijiji cha Kizota Kata ya Muungano, Kindimbachini wanajenga zahanati tangu mwaka 2013, je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Benaya Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka uliopita peke yake ambao tunaumaliza Juni 30 Serikali imejenga jumla maboma 574 ya zahanati, lakini mwaka ujao wa fedha Serikali imetanga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya ujenzi wa maboma 300 ya zahanati kuchangia nguvu za wananchi. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge tutakwenda kuona pia uwezekano wa kupeleka fedha kwenye boma hilo la zahanati, ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwanza kabisa nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kujenga Vituo vya Afya na Hospitali za Wilaya tena nzuri za kisasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Kata ya Luguru ni kata yenye idadi ya watu wengi, kituo cha afya kikijengwa Kata ya Luguru kitahudumia Kata ya Sawida na Kata ya Kinamweli. Je, Serikali ina mpango gani wa kuharakisha ujenzi wa kituo cha afya Kata Luguru?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; vituo vya afya vya Mkoa wa Simiyu na hospitali za wilaya tuna upungufu wa vifaa tiba na Watumishi.

Je, ni lini Serikali itatuletea vifaa tiba vya kutosha na watumishi wa kutosha? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, kwamba tayari Serikali ilishamwelekeza Katibu Tawala wa Mkoa na Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu pia na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Itilima kuwasilisha maombi ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Luguru ili tuweze kuandaa fedha kwa ajili ya kwenda kuanza ujenzi katika kituo hicho cha afya.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali imeendelea kupeleka vifaa tiba pia imeendelea kuajiri watumishi wa sekta ya afya na kuwapeleka katika Halmashauri zetu kote na Halmashauri ya Wilaya ya Itilima ni moja ya Halmashauri ambazo tayari zimepelekewa zaidi ya shilingi bilioni moja ya fedha kwa ajili ya vifaa tiba. Pia imeshapelekewa Watumishi wa Sekta ya Afya na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kila mara ambapo fedha itapatikana itaendelea kupelekwa kwa ajili ya vifaa tiba, lakini pia Watumishi wataendelea kupelekwa Itilima, ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE; Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, Kata hizi mbili ambazo nimezitaja na vituo vya afya ambavyo nimevitaja vina wananchi wengi na vinahudumia wananchi wengi sana katika vituo hivi.

Je, Serikali sasa haioni sababu za kuwa na mpango wa haraka ili kuharakisha ujenzi wa wodi hizi ambazo nimezitaja ili wananchi waweze kupata huduma wasisafiri umbali mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ni kweli Kituo cha Afya cha Lukungu na Kiloleli ni miongoni mwa vituo vya afya ambavyo vinahudumia wananchi wengi sana na kwa kutambua hilo, tayari Serikali imekwishaainisha vituo vya afya vyote ambavyo vina miundombinu pungufu na vinahudumia wananchi wengi ili fedha iweze kutafutwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunaongeza miundombinu ambayo inapungua.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Songe kwamba Kituo cha Afya cha Lukungu tayari kimeingizwa kwenye mpango huo na mara fedha ikipatikana tutahakikisha tunaenda kujenga miundombinu hiyo, ahsante
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, ninashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa idadi ya walimu wanaojitolea ni wengi na ajira zinapotoka huwa hawapati nafasi ya kuajiriwa hawa ambao wamejitolea. Halmashauri yangu ina zaidi ya walimu 60 ambao wamejitolea na waliopata ajira wamepata walimu watatu tu.

Je, Serikali haioni kwamba inavunja moyo wale walimu wanaojitolea na wanaopata ajira ni wale ambao wapo mitaani? Tunataka tupate mwongozo sahihi wa Serikali na majibu stahiki kwa wale ambao wanajitolea. (Makofi)

Swali la pili, kuna tabia ambayo imejengeka ajira zinapotolewa Halmashauri ambazo ziko vijijini zinapokea watumishi ndani ya miezi mitatu wale watumishi wote wanarudi maeneo ya mijini; Serikali haioni hii tabia ambayo imejengeka ni tabia ambayo inakuja kuua mfumo wa elimu au utumishi wa umma kwenye maeneo ya vijijini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali imeendelea kuajiri watumishi wote bila kujali wanaojitolea na ambao hawajitolei. Changamoto ya kuajiri walimu wanaojitolea ilitokana na utaratibu ambao haukuwa rasmi wa kuwasilisha majina ya walimu wanaojitolea. Kwa sababu baadhi ya Wakuu wa Shule wasio waaminifu walikuwa wanatumia fursa hiyo kuingiza majina ya walimu ambao hawajitolei na mara nyingine wanaachwa walimu wale ambao wanajitolea.

Mheshimiwa Spika, kwa kutambua hilo Serikali imeandaa mwongozo mahsusi na imeandaa mfumo ambao walimu wenyewe wataingia online kuji-register, kujiandikisha kwamba ni walimu wanaojitolea katika shule fulani na Serikali itafanya uhakiki na kuthibitisha kwamba walimu wale wanajitolea katika maeneo hayo. Hii itasaidia mara ajira zinapojitokeza kuona nani amejitolea kwa muda mrefu apate kipaumbele cha kupata ajira hizo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hili jambo linafanyiwa kazi seriously na Serikali itahakikisha kwamba linakamilika mapema iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na walimu pia watumishi wa sekta nyingine ambao wanapangiwa katika Halmashauri za Vijijini na kuhama, kwenye utaratibu wa ajira kwa mfumo wa kieletroniki kwa sasa, tumeshaelekeza kwamba watumishi wote wa elimu au wa afya wakishaajiriwa kwenye Halmashauri hawatakiwi kuhama ndani ya angalau ya miaka mitatu tangu kuajiriwa. Unless kuna sababu ya msingi sana ya kulazimisha watumishi hao kuhama. Kwa hiyo, nitumie nafasi hii kwanza kuwaomba Waheshimiwa Wabunge wale maeneo ambayo kuna watumishi ambao waliajiriwa maeneo ya vijijini na wamehamishwa kabla ya umri huo tupate taarifa hizo. Tumeshapata Ludewa tumeshapata maeneo mengine, tumeanza kushughulikia na watarejeshwa katika Halmashauri zilezile ili waendelee kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili tunalifanyia kazi, ahsante. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru, nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa, Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi, iliyoko Wilaya ya Mbeya yenye watu zaidi ya laki moja iliishapita vigezo vyote vya vikao vyote vya DCC, RCC na hata kiuchumi iko vizuri. Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mbalizi itapanda kuwa Halmashauri ya Mji?

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tano, aliagiza hata kubadili Jina la Jimbo la Mbeya Vijijini. Je, ni lini Serikali itabadili jina la Jimbo la Mbeya Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Njeza Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji Mdogo wa Mbalizi ni kweli kwamba ni mamlaka ya Mji ya muda mrefu lakini tayari imeshafikisha vigezo kwa maana ya idadi ya watu, uwezo wa kiuchumi, lakini wameshafuata taratibu na kuwasilisha ofisi ya Rais TAMISEMI. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Rais – TAMISEMI sasa tunafanya tathmini lakini pia tunatambua vigezo hivyo na baadaye tutatawakilisha kwa mamlaka husika ili hatua stahiki ziweze kuchukuliwa kwa kadri itakavyokuwa inafaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusiana na jina la Halmashauri ya Jimbo la Mbeya Vijijini kubadilishwa ni taratibu ambazo zinafanywa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi, kwa hivyo Ofisi ya Rais – TAMISEMI tumechkua hili tutashirikiana na Wizara husika kuona uwezekano wa kutekeleza maelekezo hayo ya Mheshimiwa Rais.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa, Mheshimiwa Naibu Waziri, amezungumza kwamba moja ya vigezo vya kupata Halmashauri ni maombi ya Halmashauri husika kufika TAMISEMI. Halmashauri ya Wilaya ya Kilosa imeshaomba kwa miaka mitano mfululizo kuanzisha Halmashauri katika Jimbo la Mikumi, tuna vigezo vyote ambavyo vingine vimepitiliza.

Je, ni nini kauli ya Serikali kwa wananchi wa Jimbo la Mikumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo, Mbunge wa Jimbo la Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Halmashauri ya Kilosa ina Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi, na ninafahamu kwamba vikao vya awali vya kuomba kupandishwa hadhi kuwa halmashauri ya Mji vimeanza, kwa ngazi ya DCC, lakini nafahamu kwamba RCC bado haijakaa kupitisha maombi hayo. Kwa hiyo, nimwelekeze Mkuu wa Mkoa wa Morogoro kufanya mapema suala hili ili tuweze kuona kama inakidhi vigezo hivyo baada ya kuwasilishwa Ofisi ya Rais – TAMISEMI.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru. Ningependa kujua Halmashauri ya Bunda ina Majimbo mawili ambayo Halmashauri moja ipo Jimbo la Mwibara lakini Majimbo hayakutani, yamekatwa katikati na Jimbo la Bunda Mjini. Ni lini sasa Serikali itapeleka Halmashauri ya Nyamswa kwenye Jimbo la Bunda Vijijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniface Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuhusu maombi ya kuanzisha mamlaka mpya kwa maana ya Halmashauri ya Nyamswa, nimuombe Mheshimiwa Mbunge lakini nimuelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bunda, kuanza taratibu ambazo ziko kwa mujibu wa Sheria Sura 288 na kuwasilisha Ofisi ya Rais TAMISEMI ili tuweze kufanya tathmini ya vigezo hivyo. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa majibu yake awali, lakini nina swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa, Halmashauri ya Wilaya ya Busega ni moja ya Halmashauri mpya hapa nchini na makusanyo yake ni kidogo sana.

Je, Serikali haioni sababu ya msingi ya kutenga fedha kutoka Serikali Kuu ili kuanza ujenzi wa miundombinu hii ambayo Mheshimiwa Waziri ameitaja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mkurugenzi afanye tathmini kubaini gharama zinazohitajika kujenga madarasa hayo na miundombinu hiyo na awasilishe rasmi Ofisi ya Rais – TAMISEMI ili tuweze kuona kama Halmashauri inaweza kujenga sehemu ya miundombinu hiyo, lakini eneo lingine la miundombinu, Serikali Kuu iweze kuchukua. Ahsante.

MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Singida Mjini tumekarabati na kujenga shule ya Sekondari ya Mungumaji na kila kitu kiko tayari na tumeomba ili kuweze kupandishwa hadhi kuwa Kidato cha Tano na Sita lakini mpaka sasa kibali hicho hakijatoka.

Je, ni lini Serikali itatoa kibali cha kuhakikisha sasa tunaanza shule ya Kidato cha Tano na Sita pale Mungumaji Sekondari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mussa Sima, Mbunge wa Jimbo la Singida Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ninampongeza Mheshimiwa Sima na Manispaa ya Singida Mjini kwa kufikia hatua hiyo kukamilisha vigezo vinavyohitajika na nimhakikishie Ofisi ya Rais TAMISEMI, tumelichukua hili na baada ya hapa nitafuatilia nione wapi tumekwama ili shule zianze huduma mapema. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Shule ya Sekondari Lemira ina hekta 20 lakini ina madarasa toshelevu kabisa ya kuweza kuanzisha Kidato cha Tano na cha Sita.

Je, ni lini Serikali itaipandisha hadhi shule hii ya Lemira kuwa Kidato cha Tano na cha Sita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa kufuatilia kama Halmashauri ya Hai imekwishawasilisha maombi hayo kwa Kamishina wa Elimu lakini baada ya kupata ripoti ya Mdhibiti wa Kanda wa Elimu. Kama hiyo imekwishafanyika, nitawasiliana na yeye baada ya Kikao hiki ili tuweze kuona namna gani tunalisukuma hili liweze kukamilika mapema.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi, tofauti na shule ya Changarawe ambayo Serikali mmekuwa mkitusaidia sana. Shule ya JJ Mungai ambayo ni ya Kidato cha Kwanza mpaka cha Sita kimekuwa na uhitaji wa mabweni na uboreshaji wa miundmbinu yake.

Je, Serikali mko tayari kutusaidia kama mlivyofanya shule ya sekondari Changarawe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, majengo yetu au miundombinu yote katika shule zetu kwanza tunayo bajeti ya kumalizia majengo ambayo yameanzishwa na wananchi kwa maana ya maboma, kwa kutumia EP4R na tumeendelea kufanya katika miaka yote na mwaka huu pia. Pia kwa sekondari tunayo bajeti ya SEQUIP lakini tunakwenda kutekeleza mpango wa BOOST. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika eneo hilo kwanza tutakwenda kuona majengo yanayohitajika, lakini tuone gharama zake, kwa kushirikiana na mapato ya ndani ya Mji wa Mafinga na Ofisi ya Rais TAMISEMI itaona namna gani tunaweza tukatoa fedha kwa ajili ya kazi hiyo.(Makofi)
MHE. HAMIS M. MWINJUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri. Kwenye Jimbo la Muheza, Serikali iliahidi kupeleka Shilingi Milioni 600 kwa ajili ya shule mbili za sekondari kwenye Kata mpya. Kata moja ya Makole haijapata hata shilingi moja mpaka hivi tunavyoongea na mwaka wa fedha unakaribia kuisha.

Je, Serikali ina mpango wowote wa kupeleka fedha hizi kama ilivyoahidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamis Mwinjuma, Mbunge wa Jimbo la Muheza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa sekondari mpya katika Kata ambazo hazina sekondari unaendelea na kwa awamu ya kwanza Serikali ilipeleka Shilingi Milioni 470 katika Kata hizo, na itakwenda kumalizia Shilingi Milioni 130 kukamilisha Milioni 600. Ninamhakikishia Mheshimiwa Mbunge kama Kata hii ya Makole haipo kwenye orodha ya kupata Milioni 600 na haijapata, tutafuatilia tuone ni kwanini haijapata ili iweze kupata kama ipo kwenye orodha ya kupata shule hizo.(Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri zetu mbalimbali hapa nchini kuna nguvu za wananchi zimetumika kujenga shule kwenye level ya shule za msingi na shule za sekondari, zimebaki kama maboma kwa muda mrefu bila ukamilishaji.

Je, Serikali sasa kwanini isizitake Halmashauri, izitambue na kuwapa timeframe wa ukamilishaji wa majengo hayo ambayo ni nguvu za wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa nia njema ya kuhakikisha kwamba maeneo yetu yote yanakuwa na shule za msingi kwa maana ya vijiji lakini na shule za sekondari kwenye Kata, ilihamasisha nguvu kazi za wananchi lakini Serikali inachangia nguvu zile kukamilisha maboma ya madarasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya kazi kubwa sana, sote ni mashahidi kwamba fedha nyingi sana zimetolewa kwa ajili ya kukamilisha madarasa hayo katika miaka yote ya fedha ukiwepo mwaka huu, kupitia EP4R, kupitia SEQUIP lakini tunakwenda na mpango wa BOOST.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tunafahamu kwamba tungependa kuweka deadline kukamilisha maboma hayo kwa Halmashauri, lakini pia bado kuna changamoto za uwezo wa mapato ya ndani kukamilisha kwa pamoja kutoka na wingi wa majengo ambayo yamejengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba safari ni hatua, tumekwenda kwa kiasi kikubwa sana na tutakwenda kukamilisha maboma yaliyokamilika, kwa sababu mpango umewekwa vizuri kwa ajili ya shughuli hiyo.
MHE. MINZA S. MJIKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, je, ni lini sasa Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa zahanati katika Kata ya Binza Kijiji cha Iyogero?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kukamilisha kujenga zahanati katika Kijiji cha Ng’hami Wilaya ya Maswa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia kuona hatua ambazo majengo haya ya zahanati yamefikia ili tuweze kuweka kwenye bajeti kwa ajili ya kukamilisha majengo haya, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ni lini atapeleka fedha katika Zahanati ya Tiling’ati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ni kweli Zahanati ya Tiling’ati tulifika pale na wanahitaji shilingi milioni kumi kwa ajili ya ukamilishaji na Mheshimiwa Waziri wa Nchi alishaahidi kwamba fedha zitakwenda pale. Namhakikishia kwamba tutafuatilia kuhakikisha kwamba shilingi milioni kumi zinapelekwa pale Zahanati ya Tiling’ati, ahsante.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, tatizo la maboma ya zahanati nchi nzima imekuwa kero na ya muda mrefu tangu 2010, je, Serikali imefanya utafiti ni yapi yanaweza kutengenezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni kweli, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kumekuwa na maboma mengi katika vijiji vyetu kwa ajili ya zahanati lakini kwa kweli katika kipindi cha miaka hii mitatu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amekamilisha maboma zaidi ya 900. Kwa hiyo, kazi ya Serikali ni kuendelea kutambua maboma ambayo tayari yanakidhi vigezo vya kukamilishwa na fedha zinaendelea kutengwa. Mwaka huu wa fedha shilingi bilioni 90 zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma hayo.

Mheshimiwa Spika, tunafanya utafiti na tutaendelea kuyakamilisha kwa awamu, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kulingana na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri, anaonesha kwamba wananchi wanapaswa kuchangia ujenzi wa zahanati hadi kwenye maboma, lakini wapo watu ambao wamekuwa wakipita kwenye majimbo yetu wakiwaambia wananchi wasichangie ujenzi wa zahanati na maboma mengine ya elimu: Je, nini hatua ya Serikali dhidi ya hao ambao wanapotosha wananchi wasishiriki mendeleo yao? (Makofi
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Utaratibu wa ujenzi wa maboma ya zahanati kwa mpango wa maendeleo ya afya msingi upo kwa mujibu wa mwongozo wa 2007. Ni maamuzi ya Serikali kwamba wananchi wanashiriki kwa sehemu na Serikali inahitimisha. Kama wapo watu ambao wanapita katika maeneo yetu na kupingana na maelekezo ya Serikali basi naomba Serikali kwa maana ya Wakurugenzi, Wakuu wa Wilaya na Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa wawatambue watu hao ili hatua za kisheria zichukuliwe dhidi yao, ahsante. (Makofi
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Jimbo la Rungwe, wananchi wameweka nguvu sana katika kujenga maboma ya zahanati, ni lini Serikali itaongeza fedha ili kuweza kumalizia maboma hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Serikali imekuwa ikitenga fedha kila mwaka kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma na ninafahamu Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe imepata fedha zaidi ya shilingi milioni mia tatu kwa ajili ya maboma sita ya zahanati katika kipindi cha miaka miwili. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo.

Mheshimiwa Spika, pia nawakumbusha Wakurugenzi na Makatibu Tawala wa Mikoa kwamba tulitoa maelekezo lazima tuwe na uratibu wa ujenzi wa maboma badala ya kila mtu kuamua kila siku kujenga boma na mwisho wa siku maboma yanakaa muda mrefu. Wazingatie utaratibu huo kwa maana kuratibu na Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya umaliziaji, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Lini Serikali itaanza mchakato wa ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Likawage, Jimbo la Kilwa Kusini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Kata ya Likawage katika Wilaya ya Kilwa inahitaji Kituo cha Afya na Mheshimiwa Mbunge amekuwa akifuatilia mara kwa mara. Tulishaelekeza wataalamu kwa maana Mganga Mkuu wa Wilaya na Mganga Mkuu wa Mkoa, wafanye tathmini ya vigezo na kuwasilisha maombi Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Nasisitiza tupate taarifa hiyo ndani ya wiki mbili ili Mheshimiwa Waziri wa Nchi aweze kuona uwezekano wa kupeleka fedha kwa ajili ya ujenzi huo, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni lini Serikali itakamilisha Kituo cha Afya cha Migori kilichopo Kata ya Migori ambacho kimejengwa na nguvu za wananchi karibu takribani shilingi milioni 10.8 ambazo wamechangia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba kutumia fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, kumwelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Iringa pamoja na Katibu Tawala wa Mkoa wa Iringa waweze kuwasilisha maombi hayo ili tuweze kuona kama inakidhi vigezo tuweze kupeleka fedha kwa ajili ya ukarabati na ukamilishaji wa jengo hilo.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini Serikali itatupatia fedha ili tuweze kujenga Kituo cha Afya katika Tarafa ya Nangaru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, hivi sasa tayari Serikali imeanza kufanya tathmini ya pili ya tarafa ambazo hazikupata vituo vya afya vya kutosha kwa awamu ile ya pili ya mwaka wa fedha 2021/2022. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba wakati tunaendelea na tathmini hii, tutatoa kipaumbele katika Kata hii ya Nangaru kuona uwezekano wa kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya uweze kutekelezwa. Ahsante.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza. Ni lini sasa Serikali itatoa commitment ya kuibadilisha Zahanati ya Town Clinic Tabora Mjini na kuwa kituo cha afya kwa sababu inazalisha watu wengi kwa mwezi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Town Clinic katika Manispaa ya Tabora ni zahanati ya muda mrefu na inahudumia wananchi wengi sana. Serikali ilishatoa maelekezo kwa Mkurugenzi, walishaelekezwa kuandaa michoro ya ghorofa kwa sababu eneo lile ni dogo ili fedha ziweze kutengwa kwa ajili ya kujenga ile zahanati na kupandisha hadhi kuwa kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, natumia fursa hii kumkumbusha Mkurugenzi na Katibu Tawala wa Mkoa wa Tabora, kutekeleza maelekezo ya Serikali mapema ili tathmini ifanyike, fedha zitafutwe kwa ajili ya kupandisha hadhi zahanati hii kuwa kituo cha afya. Ahsante. (Makofi)
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Jimbo la Lupembe, wananchi wamejenga zahanati nyingi sana. Tunazo zahanati mpya za Welela, Havanga, Lima, Tagamenda, Ikondo na kila mahali. Pia kuna vituo vya afya kama Ikondo, Mtwango, ni vipya kabisa: Ni nini mpango wa Serikali kupeleka watumishi wa afya kwenye vituo hivi ili vianze kufanya kazi mapema? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa afya ni pamoja na kuwa na magari ya wagonjwa, Serikali ina mpango gani wa kupeleka gari la wagonjwa kwa maana ya ambulance katika Jimbo la Lupembe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nawapongeza wananchi wa Jimbo la Lupembe kwa kujitolea nguvu zao na kujenga zahanati na kuanza ujenzi wa vituo vya afya. Nampongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji mzuri. Kwa hakika Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan imeendelea kuleta fedha katika Wilaya ya Njombe na katika Jimbo la Lupembe.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa tunaongelea Kituo cha Afya cha Ikuna kinaendelea kujengwa, lakini pia zahanati zimepata fedha shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji. Vile vile watumishi wataendelea kuletwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe kwa maana ya watumishi wa kada za afya kama ambavyo zilishapelekwa 72, lakini ajira nyingine zinazofuata watatoa kipaumbele katika Halmashauri hii.

Mheshimiwa Spika, siku tatu zilizopita Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan amegawa magari ya wagonjwa 199 katika halmashauri zetu zote na magari ya usimamizi wa huduma za afya na Halmashauri ya Wilaya ya Njombe Jimbo la Lupembe limepata gari hilo. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba gari lipo njiani linafika wakati wowote kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, je, upi mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba watumishi wanapelekwa katika Kituo cha Afya cha Songwe katika Kata ya Nanyara ambacho kina upungufu mkubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali, kwanza tumeainisha maeneo yenye upungufu mkubwa wa watumishi na ajira zinazofuata tutahakikisha kituo hiki kinapatiwa watumishi wa sekta ya afya, ahsante.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Serikali imejenga vituo vya afya vitatu katika Kata ya Kaegesa, Kipeta na Kaoze: Je, ni upi mkakati wa kupeleka vifaatiba na watumishi katika vituo hivyo vya afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha huu imetenga jumla ya shilingi bilioni 69.9 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa ajili ya kupeleka kwenye vituo vya afya. Mwaka wa fedha uliopita, halmashauri zote zilipata vifaatiba. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi hili ni endelevu na tutapeleka vifaa tiba kwa ajili ya vituo hivi vya afya lakini na pia tutapeleka watumishi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba vituo hivi vinaanza kutoa huduma, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itapeleka vifaatiba katiba Halmashauri ya Itigi ambapo tumejenga zahanati na vituo vya afya lakini vifaa tiba na watumishi ni haba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Katika mwaka wa fedha uliopita, Halmashauri ya Itigi pia imepata vifaatiba, pia mwaka huu wa fedha, bajeti hii ambayo inatekelezwa, tutapeleka vifaatiba na fursa za ajira zitakapojitokeza, tutahakikisha tunatoa kipaumbele kwa watumishi ili Halmashauri ya Itigi iweze kupata huduma bora za afya. Ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mkoa wa Mtwara una zahanati sita ambazo hazijaanza kutoa huduma kutokana na kutokupata mgao wa watumishi katika ajira mpya: Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi ili kusudi zahanati hizi ziweze kuanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, tulishatoa maelekezo kwa Wakurugenzi na Makatibu Tawala wa Mikoa kwamba pale zahanati zinapokamilika, hatuna sababu ya kuziacha zisianze kutoa huduma za awali. Natumia fursa hii kwanza kumkumbusha Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo na Katibu Tawala wa Mkoa wa Mtwara kwamba watumie utaratibu wa kuwa-reallocate watumishi ndani ya halmashauri ili angalau huduma za OPD zianze kwenye zahanati hizi.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatoa kipaumbele kwenye ajira zinazofuata ili watumishi wafike katika zahanati hizi. Ahsante.
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo cha afya Nkome?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli Zahanati ya Nkome inazalisha wakina mama wengi sana kwa mwezi na inahudumia wananchi wengi kwa ujumla wake. Pia, nimhakikishie kwamba tayari imekwishaingizwa kwenye orodha ya vituo vya afya ambavyo vinatafutiwa fedha kwa ajili ya kujengwa ili iweze kutoa huduma kwa ngazi ya kituo cha afya. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Pamoja na kwamba Serikali imekuwa ikipeleka vifaa tiba kwenye baadhi ya zahanati zetu na vituo vya afya lakini bado kuna tatizo la vifaa tiba hivyo kukosa watumiaji (wataalamu). Nini kauli ya Serikali kupeleka watumishi kwenye hizi zahanati na vituo vya afya ambavyo vina vifaa tiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa na upungufu wa wataalamu wa kutumia baadhi ya vifaa tiba ambavyo vimepelekwa katika vituo vyetu. Kwa kulitambua hilo, Serikali imeandaa utaratibu wa mafunzo ya muda mfupi wa miezi mitatu mpaka miezi sita kwa wataalamu wa mionzi na wataalamu wengine ili tuweze kuziba hili gap la wataalamu wa kutumia vifaa hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, wataalamu hao tayari wamekwishaingia katika ngazi ya masomo na tunahakikisha mapema iwezekanavyo wakihitimu wanapelekwa kwenye vituo vyetu ili waweze kutumia vifaa hivyo ipasavyo. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kituo cha Afya cha Chikolopola kina mtumishi mmoja tu. Lakini pia Zahanati ya Mputeni na zahanati ya Makanyama haina watumishi kabisa. Ni lini Serikali itapeleka watumishi katika maeneo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kama ambavyo katika mwaka wa fedha uliopita halmashauri hii ya Masasi vijijini walipata watumishi. Nafahamu kwamba bado wanaupungufu mkubwa katika Kituo cha Afya cha Chikolopola. Nimhakikishie kwamba tutatoa kipaumbele kwenye ajira zitakazofuata ili waweze kupata watumishi wa kutosha katika eneo hilo. ahsante.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pale Jimbo la Kinondoni, kwa kupitia fedha za mfuko wa Jimbo tumejenga jengo la mionzi kwa maana ya (Radiology).

Je, Serikali iko tayari sasa kutupatia vifaa tiba kama vile x-ray, ultrasound pamoja na wafanyakazi ili kituo kile kiweze kuanza kazi? Nakushukuru
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kutenga fedha kupitia Mfuko wa Jimbo na kujenga Jengo la mionzi na nafahamu amekuwa akifuatilia mara kwa mara. Nimhakikishie kwamba Serikali itashirikiana na halmashauri ya Kinondoni kupitia mapato ya ndani ili waweze kununua baadhi vifaa tiba ambavyo viko ndani ya uwezo wao kama ultrasound, wakati Serikali kuu inaangalia uwezekano wa kupata fedha kwa ajili ya x-ray ili wananchi wapate huduma bora, ahsante.
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa mujibu wa taarifa ya CAG iliyotoka mwezi Machi, 2023. Halmashauri 106 zilikuwa na idara na vitengo ambavyo vinaongozwa na watumishi 747 wasiokuwa na sifa. Matokeo yake ufanisi ni duni. Ni lini Serikali itaenda kuziba nafasi hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya halmshauri ambazo zina wakuu wa idara na vitengo ambao hawajathibitishwa. Kwa sababu hizo Serikali inafanya utaratibu ikiwemo upekuzi lakini pia kuwatafuta wenye sifa za kuweza kujaza nafasi hizo ili waweze kutekeleza majukumu yao ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali iko kazini. Tunafanya vetting ya wataalamu wenye sifa hizo ili waende kujaza nafasi za wakuu wa idara na waweze kutoa huduma ipasavyo. Ahsante.
MHE. OMARI M. KIGUA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi kwa mwaka wa fedha 2024/2025 inatarajia kutenga au itatenga shilingi milioni 100 kwa ajili ya kumalizia Kitua cha Afya cha Kilindi asilia na shilingi milioni 40 kwa ajili ya hospitali ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, sasa, nataka tu nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri, hizi taarifa za kwamba tumetenga shilingi milioni 100 kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Zahanati ya Masagalu amezipata wapi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali imekuwa na utaratibu wa kuhamasisha wananchi kujenga majengo na wao kutenga milioni 50. Je, Serikali haioni iko sababu ya kutenga milioni 50 na kuwapelekea wananchi wa Masagalu na kumalizia majengo haya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo ameendelea kuweka kipaumbele katika Baraza la Madiwani ili kuhakikisha kwamba wanatenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya ukamilishaji wa majengo ya Zahanati na Vituo vya Afya.

Mheshimiwa Spika, Serikali ni moja. Mkurugenzi wa halmashauri, Katibu tawala wa mkoa wana wajibu wa kupokea maelekezo kutoka katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI, hasa tunapoona vigezo vya ukamilishaji wa majengo hayo vinakidhi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa mujibu wa jengo hili ambalo lina zaidi ya miaka mitano halijakamilika, tumemwelekeza Mkurugenzi na amechukua hiyo commitment kwamba, atenge milioni 100 kama kipaumbele katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 kukamilisha boma hili ambalo lina muda mrefu na baadaye tutaendelea na maboma mengine.

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali ina utaratibu wa kutenga milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha maboma na Halmashauri hii ya Kilindi imekuwa ikipata fedha hizo. Pia, nimhakikishie tu kwamba tutaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuhakikisha tunachangia ukamilishaji wa zahanati hiyo. Ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, toka Desemba, 2022 Mheshimiwa Rais amepeleka milioni hamsini hamsini kwenye maboma ya zahanati. Mpaka leo hayajakamilika ikiwepo Zahanati ya Mpasilasi kwenye Jimbo la Korogwe vijijini. Je, ni upi mkakati wa Serikali sasa kuhakikisha wanakwenda kusimamia ili maboma yale yakamilike?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Serikali inapeleka milioni 50 kwa ajili ya kukamilisha maboma kwenye maeneo ya halmashauri zetu ambako kuna viongozi. Kuna wakuu wa idara, Wakurugenzi, wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa. Sasa, ni wajibu wao kuhakikisha kwamba, fedha hizi ambazo Mheshimiwa Rais anazipeleka zinafanya kazi kwa wakati na kukamilisha ujenzi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, nittumie fursa hii kuwakumbusha Wahesjhimiwa wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, Makatibu tawala wa mikoa pamoja na wakurugenzi kwamba, ni wajibu wao na sisi tutafuatilia kuona maboma haya yanakamilika kwa wakati na kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali dogo la nyongeza. Kila mwaka Serikali imekuwa ikiahidi kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia kituo cha afya cha Bweri. Sasa ni lini tutapata hizo fedha ili kile kituo kiweze kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bweri tayari kimeingizwa kwenye orodha ya vituo vya kimkakati ambavyo vinatafutiwa fedha kwa ajili ya ukamilishaji. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge awe mvumilivu, aamini kwamba Serikali ipo kazini na mara fedha itakapopatikana tutahakikisha kwamba tunaipeleka kwa ajili ya kukamilisha Kituo cha Afya cha Bweri. Ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi wa nyumba ya Mganga katika Zahanati ya Kijiji cha Mchalambuko Wilayani Kilwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutafanya tathmini ya mahitaji ya gharama zinazohitajika kwa ajili ya ukamilishaji wa nyumba ya mtumishi. Lakini tutatafuta fedha kwa kupitia mapato ya ndani, lakini pia na Serikali Kuu ili nyumba hiyo ikamilike na watumishi wetu waweze kuishi pale. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wakati wa Bunge la Bajeti niliahidiwa shilingi milioni 500 kwa ajili ya uboreshaji wa vituo vya Kalenge na Nyubusozi wilayani Biharamulo. Ni lini pesa hiyo itatumwa ili huduma hiyo iweze kufanyika kwa ajili ya wananchi wa Biharamulo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Vituo hivi vya afya ambavyo viliahidiwa katika Bunge la Bajeti, ni sehemu ya kipaumble cha Serikali katika kuhakikisha kwamba tunatafuta fedha na kuzipeleka ili ujenzi uweze kufanyika. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Mbunge uwe na Subira kidogo wakati Serikali inatafuta fedha na mara fedha zikipatikana kwa awamu tutahakikisha kwamba tunaanza ujenzi wa vituo vya afya katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni lini Serikali itapeleka fedha za kumalizia Zahanati ya Kidanda katika Kata ya Itwangi – Shinyanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nielekeze halmashauri husika iweze kuleta taarifa ya hatua ya ujenzi wa boma hilo la zahanati ulipofikia, ili liweze kuingizwa kwenye mpango wa kutafutiwa fedha kwa ajili ukamilishaji wa jengo hilo. ahsante.
MHE. KASALALI E. MAGENI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kutosha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Zahanati katika Kijiji cha Chamva ili hali fedha iliyokuwa imetumwa awali haikutosha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, maeneo yote ambayo Serikali ilipeleka milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma, kwanza maelekezo ilikuwa ni kwamba boma liwe limefikia hatua ya linter. Pia, kwa tathimini zetu kwa kiasi kikubwa milioni 50 ilikuwa inatakiwa kukamilisha boma. Sasa kama eneo hili la Chamva fedha ilipelekwa lakini boma halikukamilika, kwanza tunataka Mkurugenzi wa Halmashauri atupatie taarifa rasmi kwa nini milioni 50 hazikutosha kukamilisha boma, tujiridhishe na matumizi sahihi ya fedha hizo.

Mheshimiwa Spika, pili, wanatakiwa kutenga fedha kwenye mapato ya ndani ili kuhakikisha kwamba wanakamilisha jengo la Zahanati ya Chamva. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mimi katika Jimbo langu la Sikonge, wananchi pamoja na Mfuko wa Jimbo tumeshirikiana. Tuna maboma 14 ambayo yanahitaji milioni hamsini hamsini, jumla milioni 700 na halmashauri haina uwezo. Je, Serikali kuu haiwezi kutusaidia tuweze kumaliza maboma hayo 14.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Safari ni hatua, Serikali imeendelea kupeleka fedha katika Jimbo la Sikonge kwa ajili ya umalizaji wa maboma. Nimhakikishie kwamba tutaendelea kwa awamu kutafuta fedha ili kuendelea kukamilisha maboma haya. Ahsante.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Kwa muda mrefu Jimbo la Kibamba halijapata fedha hizi za mambo na ninayo maboma ya zahanati ya Saranga King’azi na Msakuzi. Je, ni lini Serikali inaweza kuweka commitment hasa kwa mwaka huu 2023/2024 ili waweze kuleta fedha tumalizie maboma haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Maboma ya zahanati katika Jimbo la Kibamba Halmashauri ya Ubungo yatatafutiwa fedha kwa ajili ya ukamilishaji. Hata hivyo, nitumie fursa hii kuwakumbusha wakurugenzi wa Manispaa zenye mapato makubwa kama Ubungo na Manispaa nyingine, kuweka kipaumbele cha fedha za miradi ile asilimia 40,60 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma hayo wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma hayo. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini sasa Serikali itatuletea fedha za kujenga chumba cha maiti na jengo la emergence katika Kituo cha Malawi katika Kata ya Vituka ukizingia sasa Temeke hospitali ni ya kimkoa na si kituo tena.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, mpango wa Serikali ni kuhakikisha kwamba huduma zote za msingi zinapatikana katika maeneo ya vituo vya huduma ikiwemo majengo haya ya mortuary na majengo ya dharura. Ndiyo maana mwaka 2022 majengo ya dharura zaidi ya 80 yamejengwa, majengo ya ICU yamejengwa.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo, naomba nitumie fursa hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutafanya tathimini ya majengo hayo tujue gharama zake lakini pia tuone mapato ya ndani yatachangia kiasi gani na Serikali kuu itachangia kiasi gani. Ahsante.
MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, kwa kuwa kituo hiki kinahudumia zaidi ya Kata tatu na wananchi wanalazimika kutembea zaidi ya kilometa kumi kutafuta huduma hizi za Mama na Mtoto.

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwenye Kituo cha Afya Loliondo ili basi ujenzi wa jengo la Mama na Mtoto liweze kujengwa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, wananchi wa Kata ya Songoro katika Wilaya ya Meru wamejitolea kwa nguvu zao binafsi kujenga jengo la Kituo cha Afya hadi kufikia kwenye ngazi ya lenta.

Je, ni lini Serikali itawasaidia wananchi hawa kumalizia kituo hiki cha afya ambacho kitakwenda kuhudumia zaidi ya wananchi 10000? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Loliondo kinahudumia wananchi wengi wa ndani ya Kata tatu. Pia ni kweli kwamba wananchi wanalazimika kutembea umbali mrefu.

Mheshimiwa Spika, dhamira ya Mheshimiwa Rais Dkt Samia Suluhu Hassan ni kupunguza umbali wa wananchi kufuata huduma za afya. Ndiyo maana tayari kituo hiki cha Afya cha Loliondo kimeingizwa kwenye orodha ya vituo 199 vinavyotafutiwa fedha. Vile vile, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatoa kipaumbele kwenye kituo hiki cha afya ili kiweze majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, pili, niwapongeze wananchi wa Kata ya Songoro Halmashauri ya Meru kwa kuanza kwa nguvu zao kujenga majengo ya Kituo cha afya. Tutakwenda kufanya tathmini kuona ni kiasi gani cha fedha kinahitajika ili tuweze kutafuta fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa kituo cha afya cha Songoro. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kupata maswali mawili ya nyongeza.
La kwanza, mara baada ya mgogoro huo kutatuliwa, Shule ya Msingi Bondo iliyokuwa Handeni Mjini tumeikabidhi Kilindi, na Shule ya Msingi Parakwiyo iliyokuwa Kilindi imekabidhiwa Handeni Mjini. Swali langu ni kwamba, ni lini sasa Sereikali itaweka utaratibu wa walimu wa shule hizi mbili kuhamishiwa kwenye halmashauri husika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuambatana na mimi mara baada ya Bunge hili kwenda Kata ya Kwamagome kwenye eneo linaloitwa Kwaubaka ambako sasa baada ya kuikabidhi Shule ya Msingi Bondo kwenda Kilindi, tumeanza jitihada za kujenga shule nyingine ili akajionee jitihada za wananchi na waone namna gani Serikali watatusaidia?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Kwagilwa, kama ifuatavyo; kwanza, niwapongeza Wananchi wa Halmashauti ya Handeni pamoja na Kilindi kwa kutatua mgogoro huu na nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kusimamia suala hilo kwa umakini mkubwa.

Mheshimiwa Spika, nimuhakikishie tu kwamba tumeshatoa maelekezo kwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Tanga, kuhakikisha ifikapo tarehe 30 Desemba mwaka huu Watumishi wote wa shule ya Bondo na Parakwiyo wawe wamepewa barua zao za uhamisho kulingana na eneo ambalo wanatakiwa kuwa katika halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Spika, pili, niko tayari kuambatana na Mheshimiwa Mbunge kwenda kuona juhudi za wananchi na kuona namna gani Serikali itawaunga mkono. Ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Mgogoro kati ya mpaka wa Mkoa wa Singida na Mkoa wa Tabora kwenye Wilaya za Uyui na Sikonge upo tangu mwaka 2002 na mwaka 2009 wataalamu walikubaliana kuchora upya huo mpaka. Sasa je, ni lini Serikali itaweka hizo beacons kutenganisha hii mipaka ya Mkoa wa Tabora na Mkoa wa Singida ili kuondoa hiyo migogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Natumia fursa hii kuwaelekeza Wakuu wa Mikoa ya Tabora na Singida kuhakikisha wanatekeleza maelekezo ya Serikali ya kutatua migogoro ya mipaka kati ya wilaya na wilaya, lakini kati ya mkoa na mkoa ili wananchi waweze kufanya kazi kwa utulivu na amani.

Mheshimiwa Spika, tutafuatilia hilo kwa Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa hii miwili, nakuhakikishia kwamba Ofisi ya Rais TAMISEMI, itahakikisha beacons hizo zinawekwa na kuhakikisha kwamba wananchi wanatambua mipaka yao na kufanya kazi zao kwa amani. Ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa hii fursa. Tatizo la mpaka lipo kule kwetu kati ya Wilaya ya Arumeru Mashariki, Hai na Siha, eneo lile linasemekana ziko GN kama tatu. Je, Serikali inasemaje kuhusu mpaka halisi wa Arumeru Mashariki, Siha na Hai?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Utaratibu wa mipaka unaainishwa kwa mujibu wa GN zinazotambullika rasmi na Serikali. Kiutaratibu GN ya mwisho ndiyo GN ambayo inatambulika, GN ambayo imepitishwa kwa mara ya mwisho ndiyo GN ambayo ina-sound kwa kipindi hicho.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue jambo hili la Mheshimiwa Pallangyo ili tuweze kuongea na Mkuu wa Mkoa wa Arusha lakini na Kilimanjaro ili waweze kuona namna nzuri ya kwenda na wataalamu kusoma GN uwandani, kutafsiri mipaka ya Wilaya ya Hai, Siha Pamoja na Arumeru Mashariki ili wananchi watambue mipaka hiyo lakini pia waweze kufanya shughuli zao kwa amani zaidi, ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba sasa kupata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Hospitali hii ya Kaloleni inahudumia wananchi wengi wa Jiji la Arusha lakini Kituo hiki cha Afya kina watumishi saba ambao wamefanya kazi kwa muda mrefu sana kwa mkataba.

Je, Serikali haioni sasa ni wakati muafaka wa kuwapa watumishi hawa ajira ya kudumu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa mtaani kuna wahitimu wengi wa kada hii wamekuwa wakisubiri ajira Serikalini na binafsi, je, Serikali haioni umuhimu wa kuwatumia wahitimu hawa wa hii Kada ya Afya wafanye kazi kwa kujitolea kwa sababu tuna upungufu mwingi katika sekta hii baadaye waje wapewe ajira rasmi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Catherine Magige, kama ifuatavyo:-

Kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amekuwa akifuatilia huduma za afya kwa wananchi wa Mkoa wa Arusha. Namuhakikishia tu kwamba tunatambua kwamba Kituo cha Afya cha Kaloleni kinahudumia wananchi wengi lakini pia kina watumishi wanaojitolea ambao wapo pale kwa mkataba na Jiji la Arusha.

Mheshimiwa Spika, namhakikishia tu kwamba Serikali imeweka utaratibu mzuri wa kutoa kipaumbele cha ajira kwa watumishi ambao wanajitolea. Tutahakikisha pia watumishi hawa kama vigezo vyao kwa maana ya umri tangu wamehitimu vyuo uko ndani ya kipindi ambacho tunaajiri, basi tutahakikisha kwamba tunawapa kipaumbele ili waweze kupata ajira za kudumu.
Mheshimiwa Spika, pili, tayari Serikali ishatoa Mwongozo wa wahitimu wote wa kada mbalimbali za afya kuomba kujitolea kwenye vituo vyetu vya huduma za afya na Wakurugenzi ambao wana mapato wanaoweza kuwalipa, wawaajiri kwa mikataba waendelee kutoa huduma wakati wanasubiri ajira za kudumu. Jambo hili, namuhakikishia Mheshimiwa Mbunge, Serikali itaendelea kulisimamia kuhakikisha kwamba wataalamu hao wanajitolea katika maeneo hayo, ahsante. (Makofi)
MHE. NJALU D. SILANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tatizo lililoko Karatu linafanana kabisa na tatizo lililoko Wilaya ya Itilima. Zaidi ya zahanati 10 tumepata vibali lakini hatuna watumishi kada ya afya, nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Njalu, Mbunge wa Jimbo la Itilima kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Halmashauri ya Wilaya ya Itilima ni moja ya halmashauri nchini zenye upungufu mkubwa zaidi wa watumishi ukilinganisha na halmashauri nyingine.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, katika ajira za watumishi wa sekta ya afya ametoa kipaumbele katika Halmashauri na Mikoa yenye upungufu mkubwa zaidi wa watumishi ikiwemo Mkoa wa Simiyu na ikiwemo Halmashauri ya Itilima.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, kama ambavyo ajira zilizopita wamepata kipaumbele cha watumishi wengi, mara fursa za ajira zitakapojitokeza tutahakikisha tunapeleka watumishi wengi zaidi Itilima ili wapate kutoa huduma bora za afya kwa wananchi, ahsante.
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Spika, ahsante, niungane na wenzangu tatizo lililopo kwenye mikoa yao, hususani katika Mkoa wetu wa Tabora hasa kwenye zahanati za pembezoni kwenye wilaya pamoja na kwenye manispaa, watumishi wa afya ni wachache sana.

Mheshimia Spika, ni lini Serikali itatuletea watumishi wa afya wa kutosha kwenye zahanati na vituo vyetu vya afya katika Mkoa mzima wa Tabora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa hakika Waheshimiwa Wabunge lakini na Wananchi wa Tanzania kwa ujumla ni mashahidi kwamba Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan katika kipindi cha miaka hii mitatu, ameajri watumishi wengi sana wa Kada za Afya na kuwapeleka kwenye vituo vyetu vya huduma za afya.

Mheshiwa Spika, zoezi hili ni endelevu, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Munde kwamba, mara ajira za Kada mbalimbali za afya zitakapojitokeza, tutahakikisha pia tunatoa kipaumbele katika Mkoa wa Tabora lakini hasa katika vituo ambavyo viko pembezoni na vina upungufu mkubwa wa watumishi.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Kituo kipya cha Afya ambacho kipo katika Kata ya Misha katika Manispaa ya Tabora Mjini kina upungufu mkubwa wa watumishi lakini pamoja na vifaa. Sijui Serikali inajipangaje kukisaidia kituo kile?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini, kama ifuatavyo. Katika kipindi cha mwaka huu wa fedha 2023/2024, tayari Manispaa ya Tabora imeshapokea zaidi ya shilingi 750,000,000 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika vituo vya huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, nimuhakikishie kwamba, katika eneo la vifaatiba, Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuhakikisha vituo vyetu vilivyokamilika lakini na vituo vya zamani vinapata vifaatiba vya kutosha kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kituo ambacho amekitaja kina upungufu wa watumishi lakini kama ilivyo utaratibu wa Serikali, tunaendelea kupeleka watumishi kwa awamu, na tutahakikisha pia kituo kile kinapata watumishi ili waweze kutoa huduma bora zaidi kwa wananchi, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna majibu mengine yanasikitisha sana. Kituo cha Mugeta kimeisha mwaka 2019, wakati kituo hiki tunajenga tulipewa shilingi milioni 700, siyo kwamba hela zinatafutwa hapana, shilingi milioni 700, shilingi milioni 400 wakasema tujenge majengo kwa kushirikiana na wananchi na shilingi milioni 300 zinaenda MSD vifaatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoenda kufuatilia mwaka 2020 tukaambiwa vifaatiba vitakuja vya shilingi milioni 161 na vimeshakuja. Wakasema vifaa vingine vya shilingi milioni 139 viko njiani, leo unaambiwa kuna bajeti inatengwa, hizi shilingi milioni 300 zilizoenda MSD ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua tutatengaje bajeti ambayo tayari ilishaenda? Kwa hiyo, naomba hili jokofu la Mugeta lipelekwe, fedha zipo MSD. (Makofi)
Swali la pili, tumejenga Kituo cha Afya Hunyari lakini hakina theater, sasa naomba kujua ni lini hii theater ya Kituo cha Afya Hunyari itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namwelewesha Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha za vifaatiba haimaanishi ni fedha za kununua jokofu la mochwari peke yeke. Tukikamilisha ujenzi wa kituo cha afya vifaatiba vya kipaumbele ni vifaa ambavyo vitakwenda kutibu wananchi. Vifaa vya upasuaji, vifaa vya wodini, vitanda, magodoro na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili tunakwenda kupeleka vifaa kwa ajili ya kuhifadhia maiti kwa maana ya majengo ya mochwari pamoja na majokofu. Kwa hiyo, hiyo shilingi milioni 300 ambayo ilikwenda MSD ilinunua vifaatiba ambavyo viliwezesha kituo cha afya hicho kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Mwaka huu wa fedha tayari Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshawaletea shilingi milioni 700 kwa ajili ya kununua vifaatiba vingine likiwemo jokofu la mochwari. Naomba Mheshimiwa Mbunge tuishukuru Serikali kwamba imefanya kazi kubwa, imeleta fedha nyingi za vifaatiba, jokofu litanunuliwa kati ya Februari na Machi ili wananchi wa Bunda waweze kupata huduma nzuri za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuhusu Kituo cha Afya cha Hunyari ni kweli kwamba kuna majengo ambayo yamejengwa lakini bado hatuna jengo la upasuaji. Safari ni hatua, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa awamu ili twende kukamilisha majengo mengine kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Hunyari. Ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutupatia gari la ambulance katika Kituo cha Afya cha Kinesi. Kituo cha Afya cha Kinesi kinahudumia tarafa mbili kwa maana ya vijiji zaidi ya 25. Kwa sasa tunapopata maafa Wananchi hutulazimu kusafirisha miili ya ndugu zetu hawa kwenda Musoma Mjini kwa kutumia mtumbwi ama boti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tayari tuna jengo la mochwari katika kituo hiki, ni nini mpango wa dharura kuhakikisha kwamba mnatupatia jokofu ili kunusuru na kuondoa adha wanayopata Wananchi wakati wanapopata maafa haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilipeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kinesi, kimekamilika na kinatoa huduma. Tunafahamu kwamba kituo hiki bado hakijakamilisha ujenzi wa jengo la kuhifadhia maiti na upo katika hatua ya asilimia 85. Tunafahamu pia kwamba jengo hili halijapata mashine kwa maana ya jokofu la kuhifadhia miili ya marehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Rorya kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambaye alishatoa maelekezo hayo, kwamba wahakikishe kupitia mapato ya ndani wanakamilisha asilimia 15 iliyobaki kukamilisha jengo la mochwari. Mheshimiwa Rais ameshapeleka shilingi milioni 400 kwa ajili ya kununua vifaatiba na kati ya fedha hiyo watenge hiyo shilingi milioni 32.5 kwa ajili ya kununua jokofu la kuhifadhia maiti kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kinesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema kwa ujumla, tumekuwa na hoja nyingi za Waheshimiwa Wabunge kutoka katika Majimbo yote, Mheshimiwa Rais amepeleka fedha shilingi milioni 500, vituo vya afya vimekamilika vimeanza kutoa huduma. Wakurugenzi wa Halmashauri, Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya wasimamie mapato ya ndani kukamilisha majengo ya kuhifadhia maiti katika vituo vyote ambavyo vimekamilika ili kuondoa kero hiyo kwa wananchi. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaleta fedha ni kazi ndogo ya shilingi milioni 30 tu kukamilisha yale majengo lakini pia waweke kipaumbele kununua majokofu kwa ajili ya majengo hayo katika vituo hivyo. Ahsante.(Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo kwa Getere na mimi liko kwangu Mwibara; je, ni lini Serikali itajenga majokofu katika Vituo vya Afya vya Kasaunga, Kisolya, Kasuguti na Isanju?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Kajege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaelekeza Halmashauri zetu zote kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kukamilisha majengo ya mochwari, pia kutenga fedha ambazo zinapelekwa kwa ajili ya vifaatiba kwa ajili ya kununua majokofu ya mochwari. Kwa hiyo, nakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia kuona Halmashauri ya Rorya Jimbo la Mwibara pia wanatenga na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma zinazostahili. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wananchi wa Kijiji cha Lungemba na Kitelewasi kwa kushirikiana na Halmashauri na Mfuko wa Jimbo wamejenga majengo ya mama na mtoto; je, Serikali iko tayari kuwasapoti kwa kuwaletea vifaatiba katika majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nawapongeza Wananchi wa Lungemba na Kitelewasi kwa kuchangia nguvu zao kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya huduma ya mama, baba na mtoto. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba vituo vyote ambavyo vimejengwa kwa nguvu za wananchi vikishasajiliwa Serikali inachangia nguvu zake, kwa maana ya kupeleka fedha kuhakikisha kwamba vinaanza kutoa huduma. Kwa hiyo, tuko tayari kuwaunga mkono wananchi kwa ajili ya kuanza kutoa huduma katika majengo haya, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutupatia gari la wagonjwa ambalo tumelipeleka katika Kituo cha Afya cha Umbwe. Kituo hiki cha afya kinahudumia Kata sita katika Tarafa ya Kibosho na hakina mortuary. Je, Serikali ina mpango gani wa kutusaidia kutujengea mortuary katika kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Profesa Ndakidemi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza natumia fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge na kuwapongeza kwa kupokea magari ya wagonjwa ambayo Mheshimiwa Rais amenunua kwa ajili ya Majimbo yetu na Halmashauri zetu zote kote nchini. Pamoja na hilo tunaendelea kuboresha sana huduma za mortuary, natumia nafasi hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Moshi Vijijini kutenga fedha ya mapato ya ndani kwa ajili ya jengo la mortuary na kutumia fedha ya vifaatiba kwa ajili ya kununua majokofu ili kuboresha huduma kwa wananchi, ahsante. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kiponzero ni moja ya vituo kongwe katika Jimbo la Kalenga, bahati mbaya mpaka leo hakina cha chumba cha mortuary; je, ni lini Serikali itatupa jokofu pamoja na chumba cha mortuary?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Jackson Kiswaga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza na narejea kusema kwamba maelekezo yameshatolewa kuhakikisha kwamba Wakurugenzi wanajenga majengo ya kuhifadhia maiti. Pia wananunua majokofu katika vituo vyote vilivyopo ambavyo vinatoa huduma kote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, namuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Iringa Vijijini kuhakikisha wanaanza kujenga jengo la mortuary, lakini pia wananunua jokofu kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kiponzero, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa naishukuru Serikali kwa ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali kwenye Mkoa wetu wa Morogoro. Hii Zahanati ya Uwanja wa Ndege ina upungufu wa wafanyakazi hasa manesi na madaktari. Je, ni lini mtapeleka hao Manesi na Madaktari ili kutimiza ikama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Kituo cha Afya Mafiga kimekuwa na tatizo sana la theatre na wanawake wengi wajawazito wanapenda sana kujifungulia pale, na mara wanapopata matatizo, wanapelekwa Hospitali Kubwa ambapo kuna mwendo. Je, ni lini Kituo hiki cha theatre kitajengwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Zahanati hii ya Uwanja wa Ndege ina watumishi watano; Afisa Tabibu mmoja, Wauguzi wawili, Mtaalamu wa Maabara mmoja na Mhudumu wa Afya mmoja. Kwa idadi ya wananchi ambao wanatibiwa pale, tunahitaji kuongeza wataalamu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tayari Serikali imeshaitambua Zahanati hiyo, mara ajira zitakapojitokeza, tutahakikisha tunawapa kipaumbele kwa ajili ya kuongeza idadi ya watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la pili, Kituo cha Afya cha Mafiga ni kweli kipo mjini na kinahudumia wananchi wengi na kina upungufu wa baadhi ya miundombinu ikiwepo majengo ya upasuaji na majengo mengine. Tushamwelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro kuandaa mchoro wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Mafiga. Nitumie fursa hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia ili tuweze kuona umefikia hatua gani na tuone uwezekano wa kuongeza majengo katika Kituo cha Afya cha Mafiga, ahsante. (Makofi)
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri; je, ni lini Serikali itaongeza fedha za ujenzi wa Zahanati kwenye vijiji hasa Majimbo ya Vijijini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gulamali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikijenga Vituo vya Afya katika maeneo ya vijijini kwa kuchangia nguvu za wananchi kwa kutoa shilingi milioni 50 kwa ajili ya umaliziaji. Fedha hiyo shilingi milioni 50 ilianza kutolewa mwaka 2016/2017 na ukizingatia kasi ya inflation kwa sasa, tumeshapitia bajeti za ujenzi wa Vituo vya Afya, Zahanati na pia Hospitali za Wilaya. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Serikali imeshafanya kazi hiyo ya kubadili au kuongeza kiasi cha fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati. Taarifa rasmi itatolewa na Waheshimiwa Wabunge mtaipata na fedha zinazokuja zitakuwa na mabadiliko ili kuendana na inflation iliyojitokeza, ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Baadhi ya zahanati ambazo zimejengwa Makao Makuu ya Kata hasa Sirop, Dirma, Laghanga, Getanuwas na Ishponga hazina jengo la mama na mtoto; je, Serikali ina kauli gani ili kuboresha afya ya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Samweli Hhayuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati zote ambazo zimejengwa na zina upungufu wa majengo ya Huduma za Afya ya Mama, Baba na Mtoto, tumeshatoa ramani nyingine kwa ajili ya kuongeza majengo hayo kwenye zahanati hizo ili huduma hizi ziweke kupatikana. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zahanati ambazo amezitaja hapa tutazipa kipaumbele pia kuhakikisha kwamba zinajenga majengo hayo, ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami naomba kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Zahanati ya Nahasey Wilayani Mbulu ambayo iko katika mazingira magumu hasa sehemu ya mama na mtoto na kutoa huduma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati hizi ambazo zinaendelea kujengwa katika maeneo yetu, zinatumia fedha za mapato ya ndani na pia fedha kutoka Serikali Kuu. Kwa hiyo, naichukua hoja ya Mheshimiwa Mbunge na baada ya hapa tutafuatilia kule Bunda tuone chanzo cha fedha ambacho kinaweza kupatikana mapema iwezekanavyo ili tuweze kukamilisha ujenzi wa zahanati hii yakiwemo hayo majengo ya Huduma ya Afya ya Mama, Baba na Mtoto, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama yote hayo wanayafahamu, sasa ni zaidi ya mwaka wa tatu tumesimama hapa kuomba Kituo cha Afya cha Ngerengere, hakina jengo la Huduma ya Mama na Mtoto, Mortuary hakuna. Wakazi wa Kata ya Ngerengere ni 15,000, Kata ya jirani ya Kidugalo ni 8,000, leo hii Mheshimiwa Waziri anajibu majibu ambayo anafahamu tatizo liko wapi, mpaka nashindwa kuelewa. Naomba kumwuliza swali Mheshimiwa Waziri; je, ni lini mtakwenda kutatua hili tatizo? Siyo kwamba majibu mnayo na utatuzi hakuna, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamisi Shabani Taletale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Ngerengere. Nasi kama Serikali, taarifa hii tunaifahamu na ndiyo maana tulitoa maelekezo kwa Mkurugenzi, kuongeza eneo la ujenzi wa Kituo cha Afya, ekari 4 na nusu hazitoshi kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya hiki kilikuwa ni cha Mission, kwa hiyo, kilichukuliwa na Serikali kikiwa tayari kinatoka Mission. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba mara hili eneo la ekari mbili la Posta ambalo halijaendelezwa, ambalo liko mkabala kabisa na Kituo hiki, likishachukuliwa na kuwa na ekari sita na nusu, basi mapema iwezekanavyo tutatafuta fedha kwa ajili ya kuongeza majengo haya ambayo yanapungua katika Kituo cha Afya cha Ngerengere, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Kata ya Mbande ya Chamazi katika Mkoa wa Dar es Salaam ni kata ambayo ina idadi kubwa ya watu, lakini wana Zahanati ya Mbande: Ni lini sasa Serikali itaipandisha Zahanati ya Mbande kuwa Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Mariam Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba idadi ya wananchi katika Kata ya Mbande kule Chamazi ni kubwa na Zahanati ile ya Mbande kwa kweli inazidiwa na idadi ya wananchi na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeshaainisha kwamba eneo la Zahanati ya Mbande ni sehemu ya eneo la kimkakati kuona uwezekano wa kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tunalifanyia kazi na tutahakikisha kwamba tunatafuta eneo linalotosheleza kama lile la Zahanati linatosha ama tunahitaji kupata eneo lingine kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya kwa manufaa ya wananchi walio wengi katika eneo lile, ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa mwenyekiti, wananchi wa Kata ya Kabwe wana changamoto ya kijiografia na wanapata shida kubwa sana ya matibabu kuja Hospitali ya Wilaya; na ile ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kujengewa Kituo cha Afya. Ni lini mtapeleka fedha kumalizia kujenga kituo hicho ili wananchi wapate huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi zinazotolewa na viongozi wetu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji. Kwa sababu hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na ninakumbuka nilikuwa kwenye ziara yake, nakuhakikishia tayari tumeshaingiza kwenye Mpango Mkakati kwa ajili ya kutafuta fedha na kwenda kujenga Kituo cha Afya katika Kata ya Kabwe, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa kuwa Tarafa ya Ndagalu Kata ya Ng’haya, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu ilitoa fedha kwa ajili ya kuweka miundombinu kwenye Zahanati ya Ng’haya ili kuipandisha hadhi kuwa Kituo cha Afya.

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya zahanati hiyo kuwa Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii kumsisitiza na kumkumbusha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Magu, kwamba tulishawaelekeza kwanza kufanya tathmini ya majengo yanayopungua kwenye ile zahanati ili iwe na hadhi ya kupandishwa kuwa Kituo cha Afya. Kwa hiyo, nitafuatilia Mheshimiwa Kiswaga, tuweze kuona wamefikia hatua gani kwa maana ya Mkurugenzi na timu yake, pia tuone namna gani tunapata fedha, iwe ni kwa mapato ya ndani ya Halmashauri au kwa fedha kutoka Serikali Kuu ili tuweze kupandisha hadhi hii Zahanati ya Ng’haya iweze kuwa Kituo cha Afya, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mwaka 2021 Kata ya Mgombezi kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini walipatiwa shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya. Baadhi ya majengo yalijengwa lakini mpaka sasa tunapoongea, shilingi milioni 250 za ziada hazijafika kwenye ile Kata ya Mgombezi, zaidi ya miaka miwili. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, ni lini Serikali itatuletea shilingi milioni 250 zilizobaki ili kwenda kumalizia Kituo cha Afya cha Mgombezi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna Vituo vya Afya katika Majimbo mengi hapa nchini ambavyo vilipewa shilingi milioni 250 mwaka wa fedha 2021/2022 na majengo ya shilingi milioni 250 yamekamilika, yameanza huduma za awali za OPD kwenye baadhi ya Vituo lakini kuna majengo yanayohitajika kwa ajili ya kukamilisha ngazi ya Kituo cha Afya. Naomba kumhakikishie Mheshimiwa Kimea kwamba tunatambua Vituo vyote ambavyo vimepata shilingi milioni 250 na bado shilingi milioni 250.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametupa kibali kuweka kwenye bajeti ambayo tunaanza kuipanga hivi karibuni, kuhakikisha Vituo vyote vya Afya vilivyopata shilingi 250 na bado shilingi milioni 250, vinapelekewa mwaka ujao wa fedha ili vituo vile viweze kukamilika, ahsante. (Makofi)
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana; Mji wa Mafinga ni Mji ambao unakuwa kwa kasi kubwa sana. Kuna Kituo cha Afya cha Upendo ambacho wananchi walishaanza kukijenga. Ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Tendega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inathamini nguvu za wananchi na tutakwenda kufanya tathmini ili tuone namna gani tunachangia kukamilisha Kituo cha Afya cha Upendo. Ahsante. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante; nimekuwa nikiuliza kila siku kuhusu Zahanati ya Town Clinic ambayo ina msongamano mkubwa wa watu kufikia kuzalisha wanawake 200 kwa mwezi, na Mheshimiwa Naibu Waziri amekuwa akinijibu Mkurugenzi alete michoro; je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mkakati gani wa kumwandikia sasa Mkurugenzi kwa maandishi ili aweze kuleta huo mchoro na Zahanati ya Town Clinic iwe Kituo cha Afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Munde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Munde, alikuja, tulimwita Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, tulikaa naye mimi, Mheshimiwa Mbunge na Mkurugenzi, tukampa mkakati wa kwenda kuandaa michoro hiyo aweze kuiwasilisha. Si kwa barua, bali tulimwita na tukakutana. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tuna taarifa zote za hatua ambazo zinaendelea kwa ajili ya kupandisha hadhi Zahanati ile ya Town kuwa Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora kuleta michoro ile haraka iwezekanavyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona namna gani tunaanza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Town. Ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, Zahanati ya Kijiji cha Nkome nimekizungumza humu mara tatu; inazalisha shule kila mwezi, maana yake watoto zaidi ya 550; na kwa sasa tumeenda zaidi tunafika karibia 600 kwa mwezi; mliniahidi kuongeza uwezo wa ile zahanati ili iwe Kituo cha Afya, tathmini zote zimefanyika na mwezi huu wametoka kukagua tena, na fedha ipo shilingi milioni 500; lini hiyo fedha itakuja? Lini Mheshimiwa Naibu Waziri atakuja ili akaangalie huo uzalishaji wa hiyo zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Musukuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Zahanati hii ya Nkome aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge, kwa kweli imezidiwa kwa idadi kubwa ya wananchi katika eneo lile na Serikali ishaweka mpango wa kupandisha hadhi kuwa Kituo cha Afya. Mwenyewe amesema wiki moja, mbili zilizopita wataalamu kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, walifika kufanya tathmini kwa ajili ya kutumia fedha za Benki ya Dunia kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili liko on track na tutahakikisha tunajenga Kituo cha Afya hiki mapema iwezekanavyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kituo cha Afya cha Kifura ambacho Serikali imekiri kwamba ni chakavu sana kinapokea wagonjwa wa nje 110 hadi 150 kwa siku lakini kinazalisha kinamama 120 mpaka 150 kwa mwezi. Je, kutokana na mzigo wa wagonjwa wengi ulioko katika Kituo hiki chakavu, Serikali haioni sasa iko sababu ya kuharakisha mchakato wa kuleta pesa za ukarabati wa Kituo hiki cha Afya cha Kifura? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Serikali iliahidi kumalizia ujenzi wa Kituo cha Afya cha Nyaruyoba kupitia ziara ya Mheshimiwa Makamu wa Rais mwaka 2021. Kituo hiki cha Afya cha Nyaruyoba kinahudumia takribani kata tatu ikiwemo Mkabule, Rusohoko na Kigaga iliyoko Kata ya Rugongwe. Je, Serikali haioni iko sababu ya kuharakisha kuleta pesa za kumalizia Kituo hiki cha Afya ambacho kinahudumia takribani kata nne katika Jimbo la Muhambwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nianze tu kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa namna ambavyo amefuatilia ahadi hizi za Serikali kuhakikisha kwamba zinakarabati Kituo cha Afya cha Kifura na ni kweli kituo hiki ni chakavu, kina upungufu wa miundombinu na kinahudumia wananchi wengi. Nimhakikishie kwamba katika mpango wa Benki ya Dunia hivi karibuni, hiki ni miongoni mwa vituo ambavyo vimeingizwa na tunaamini fedha zitakwenda kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Nyaruyoba ni ahadi ya Mheshimiwa Makamu wa Rais nimhakikishie kwamba tayari Serikali inaendelea kutafuta fedha na mapema iwezekanavyo fedha ikipatikana itapelekwa kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo hiki cha Afya, ahsante. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwenye Jimbo la Ndanda tuna vituo kwenye Kata ya Ndanda, Kijiji cha Chiroro, Lukuledi, Ngalole, Chikundi pamoja na Namajani. Vituo hivi vimeshakamilika ujenzi wake zaidi ya miaka miwili sasa hivi lakini hata hivyo havijafunguliwa na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwa sababu ya mapungufu madogo madogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba; je, yuko tayari kutoa maelekezo kwa Halmashauri yetu ya Masasi DC ili vituo hivi vikamilishwe na kuanza kutoa huduma kwa wananchi kwani zile shilingi milioni 50 zilizoletwa na Serikali hivi sasa majengo haya yameanza kuchakaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecil Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kuwapongeza Wananchi wa Jimbo la Ndanda kwa kujenga kutumia nguvu zao lakini Serikali iliwaunga mkono kuwapelekea shilingi milioni 50 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati hizi na vituo hivi na vimekamilika vitoe huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitumie fursa hii ya Bunge lako tukufu kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuwaelekeza Wakurugenzi wote wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuzingatia maelekezo ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwamba vituo vikikamilika vinabaki hatua ndogo ndogo za ukamilishaji, vifaatiba kwa ajili ya kuanza kutoa huduma. Ni lazima watoe kipaumbele kuhakikisha vinakamilika mapema na vinaanza kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa Wakurugenzi wote nchi nzima, lakini mahususi nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Masasi kuhakikisha vituo hivi ambavyo vimetajwa na Mheshimiwa Mbunge wa Ndanda mapema iwezekanavyo ndani ya miezi mitatu tuhakikishe vituo hivi vimekamilishwa na vinaanza kutoa huduma kwa wananchi, ahsante.

MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nipende kusema majibu ya Serikali kiukweli sijaridhika nayo kutokana na sababu zifuatazo. Serikali inatambua kwamba hizi kata zipo na ni maeneo yao kiutawala na huko nyuma hizi kata zilikuwa zinafanya uchaguzi wa kumchagua diwani na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa na kwa kuwa kwenye majibu ya Serikali imesema kwamba kuna mwingiliano wa makazi ya wakimbizi na raia lakini wakati huo huo kuna uchaguzi unafanyika kumchagua Rais lakini pia kuna uchaguzi wa kumchagua Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa swali langu ni; je, ni sifa zipi ambazo hawa raia au hawa wakazi wa eneo hili wanazo ambazo zinawafanya waweze kumchagua Rais na kuweza kumchagua Mbunge? Lakini ni sifa zipi ambazo hawa raia wanazikosa kuweza kumchagua Diwani na Wenyeviti wao wa Serikali za Mitaa na Vitongoji na Vijiji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; tunajua kabisa katika maeneo ya kata kiongozi wa kushughulikia shughuli za maendeleo katika Kata husika huwa ni Diwani; sasa kata hizi hazina madiwani. Je, ni nani msimamizi wa shughuli za maendeleo katika hizi kata au ni kuniongezea mimi Mbunge majukumu ambayo yangefanywa na madiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naomba nianze kwa kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua umuhimu wa wananchi hawa na vijiji hivi na kata hizi kuwa na viongozi wanaochaguliwa. Kwa sababu za kiusalama; maeneo yale yana mchanganyiko wa raia na mchanganyiko wa wakimbizi lakini na wale wakimbizi ambao wamepewa uraia hivi karibuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa sababu za kiusalama kuna kazi ya ziada inatakiwa kufanyika ili kujiridhisha na usalama wa wale ambao watakuja kushiriki katika shughuli za uchaguzi ili chaguzi hizo ziweze kwenda kwa mujibu wa taratibu lakini kwa kuzingatia usalama wa nchi yetu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hilo linahitaji umakini mkubwa ili twende katika njia ambayo ni salama zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la kwamba wanachagua viongozi wa Kitaifa kwa maana ya Mheshimiwa Rais lakini pia Mheshimiwa Mbunge; ni sawa lakini ikumbukwe kwamba Mwenyekiti wa Kijiji atatoka ndani ya Kijiji kile, utajiridhishaje beyond reasonable doubt kwamba yule Mwenyekiti siyo mkimbizi au ni raia ambaye bado hajapata uraia rasmi? Kwa hiyo, ndiyo maana taratibu zinaendelea na nikuhakikishie tu kwamba Serikali inaendelea na mchakato huo kuhakikisha kwamba tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji na kata hizi zina maafisa wanaoitwa Wakuu wa Makazi ya Wakimbizi ambao wale wanawajibika kutoa taarifa mbalimbali za Kiserikali kwenda ngazi ya halmashauri, wilaya na ngazi nyingine. Kwa hiyo, pamoja na kwamba hakuna madiwani na wenyeviti lakini kuna uwakilishi wa Wakuu wa Makazi ya Wakimbizi katika maeneo yale, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi. Naomba tu nijazilize hapo alipoongelea Mbunge aliyemaliza kuongea. Mtu mwenye sifa za kupiga kura za Urais ni raia wa Tanzania mwenye uraia wa Tanzania mwenye sifa za kupiga kura, maana yake ni raia amejiandikisha, ana umri wa miaka 18, ni raia wa Tanzania; sasa kama hao wana sifa za kupiga kura za Rais wametambulika kwamba ni Watanzania, kwa nini hawachagui Diwani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge hizo ni sehemu ya sifa za mpiga kura lakini kama nilivyotangulia kusema, kuchagua viongozi ngazi ya vijiji vile na ngazi ya kata zile ambazo zina mchanganyiko mkubwa wa wakimbizi na watu ambao siyo raia kunahitaji umakini mkubwa ili kulinda usalama wa nchi na Serikali inaendelea kuchukua hatua ambazo zitawawezesha sasa kwenda kufanya uchaguzi huo baada ya kujiridhisha na mazingira ya kufanya chaguzi katika maeneo hayo, ahsante.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa fursa hii kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa uwiano wa idadi ya walimu tuliopata katika shule za msingi na sekondari haulingani na walimu waliofariki, waliostaafu na waliohama kwa vibali vya TAMISEMI hivyo kufanya uhaba mkubwa kuendelea kuwepo.

Je, Serikali inaweza kutupa kipaumbele wilaya za pembezoni ikiwemo Namtumbo kutuongezea idadi ya walimu wakati inagawa walimu hao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa shule za msingi za Namtumbo tuna walimu 867 na tuna upungufu wa walimu 418; je Serikali inaweza kutuletea walimu kupunguza upungufu huo kwa sasa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwanza katika utaratibu wa ajira za walimu lakini pia watumishi wa Sekta ya Afya kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 walimu na watumishi wa afya wanaomba kwa njia ya kielektroniki lakini wanapangiwa kwa uwiano na idadi kubwa kwenda kwenye halmashauri za pembezoni zenye upungufu mkubwa zaidi wa watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali tayari imeshaanza kulifanyia kazi jambo hilo na ajira zote ambazo zitaendelea kuja zitakuwa zinakwenda kupeleka watumishi wengi zaidi maeneo ya vijijini na maeneo yenye upungufu mkubwa zaidi na Ofisi ya Rais, TAMISEMI tayari ina data base ya maeneo yote yenye changamoto kubwa zaidi ya walimu kama ilivyo Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba eneo hili la walimu tutaendelea kutoa kipaumbele katika Halmashauri hii ya Namtumbo na halmashauri nyingine zote za pembezoni likiwemo suala la upungufu wa walimu 418 ambalo kadiri ya ajira tutahakikisha kwamba tunatoa kipaumbele kupunguza gap ya watumishi katika Halmashauri ya Namtumbo, ahsante. (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; kutokana na upungufu wa walimu kuna walimu ambao wameendelea kujitolea katika shule za msingi na shule za sekondari kwa kulipwa na wananchi. Sasa ni kwa nini Serikali walau isiwape mkataba wa muda ili kuwapa motisha waendelee kufundisha wakati wakisubiri kuajiri walimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, Serikali ilikwishatoa kwanza maelekezo kwa Wakuu wa Shule lakini kwa maana ya Wakurugenzi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa kwamba wanaweza wakaajiri walimu wa kujitolea kwa muda wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kuwaingiza kwenye utaratibu wa ajira za kudumu; kwa hiyo, jambo hilo linaendelea kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna ya kuweka mikataba, Serikali imeandaa mwongozo mahususi ambao utapelekea kuandaa mfumo ambao utawezesha walimu wanaojitolea kutambuliwa rasmi kwenye mfumo kuepuka udanganyifu wa baadhi ya Wakuu wa Shule wasiowaaminifu ambao mara nyingi wamekuwa wanaleta majina kwa mfano wakati wa ajira walimu ambao wanajitolea lakini wanaleta pia walimu ambao hawajitolei. Kwa hiyo, tunataka tuwe na mfumo mahususi ambao walimu wenyewe watajisajili na Ofisi ya Rais, TAMISEMI itakwenda kuhakiki na kujiridhisha ili ajira zinapotokea waweze kupata kipaumbele cha kuajiriwa katika ajira za kudumu, ahsante.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri katika Bunge la Bajeti tulikuuliza swali la mfumo kuwakataa walimu wanaojitolea. Unaweza ukatoa ni lini Serikali itafanya haraka ili mfumo huo uweze kuwaelewa walimu wanaojitolea na waweze kupata ajira na kuachwa wakati muda mrefu wanajitolea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwamba wapo walimu ambao wamekuwa wakijitolea lakini mfumo wetu wa kuwatambua rasmi na kuthibitisha kwamba wanajitolea ili wapate kipaumbele cha ajira ulikuwa haujaandaliwa. Kwa hiyo, hivi sasa Serikali iko kwenye hatua za mwisho za kukamilisha mfumo ambao utawatambua na kuhakikisha kwamba wanaajiriwa kwa kipaumbele kila fursa zinapojitokeza, ahsante. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru; jengo ambalo linatumika sasa hivi kama OPD ni jengo la zamani na limechakaa. Kituo kile kimekuwa kikihudumia wagonjwa wengi sana. Mimi nataka kujua, kwa kutenga shilingi milioni 70 kwa mwaka, maana yake tutachukua muda mrefu kukamilisha jengo lile.

Kwa nini Serikali Kuu isipeleke fedha katika kituo hiki ili waweze kujenga OPD ya kisasa ambayo itaendana na mahitaji yaliyopo? (Makofi)

Swali langu la pili, hoja ya uzio sijajibiwa kabisa bado naendelea kuuliza, kuna mkakati gani wa kujenga uzio katika kituo kile cha afya ili kulinda mali za hospitali pamoja na watu ambao wanahudumiwa pale? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na miundombinu bora ya kutoa huduma za afya katika vituo vyetu. Ndiyo maana mwaka 2017/2018, Serikali ilipeleka shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga majengo matano. Tunafahamu kwamba Jengo la OPD ni chakavu na la siku nyingi na tumeanza na shilingi milioni 70 kwenye bajeti ijayo, mwaka 2024/2024. Hii haimaanishi kwamba hatutapeleka fedha nyingine. Kwa hiyo, naomba nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, huo ni mwanzo tu wa fedha za mapato ya ndani, wakati huo Serikali Kuu inatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha jengo hilo mapema iwezekanavyo ili liweze kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili kuhusiana na uzio, kupanga ni kuchagua. Kwa sababau tuna changamoto ya majengo ya msingi ya kutoa huduma, ni vema tukakamilisha kwanza majengo yale, yaanze kutoa huduma kwa wananchi lakini baadaye tutafuata na hatua ya uzio, ahsante. (Makofi)
MHE. ANNE K. MALECELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Kwanza nianze kuishukuru Serikali ya Chama cha Mapinduzi kwa kunipa vituo vya afya viwili, Kituo cha Afya cha Mtii na Kituo cha Afya cha Miamba. Naomba kuiuliza Serikali kwamba, hivi vituo vya afya vimekamilika na vimeshaanza huduma.

Je, Serikali mna mpango gani wa vituo vya afya vyote hivi viwili kujengewa jengo la kuhifadhi maiti kwa sababu, hivi vituo vya afya vyote viwili viko milimani sana? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nampongeza Mheshimiwa Mama Anne Kilango Malecela kwa namna ambavyo amefuatilia sana ubora wa huduma katika vituo vyake vya afya, vikiwemo vituo hivi viwili. Nimhakikishie kwamba baada ya kukamilisha majengo yale kuanza kutoa huduma kwa wananchi, tunaendelea na ujenzi wa miundombinu mingine ambayo haijakamilika yakiwemo majengo ya kuhifadhia maiti. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba lipo kwenye pipeline na litafanyiwa kazi, ahsante. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya swali la nyongeza. Kata ya Likawage katika Jimbo la Kilwa Kusini haina kituo cha afya na ipo mbali kutoka katika maeneo ya kutolea huduma, na Mheshimiwa Naibu Waziri alishatoa maelekezo kwa Mkurugenzi aandike andiko ili litumwe Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Andiko hilo tayari limekamilika, sasa tunataka kupata commitment ya Serikali, lini Kituo cha Afya Likawage kitajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge. Ni kweli alishafuatilia mara kadhaa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kuhusiana na ujenzi wa kituo cha afya katika kata hiyo na tayari Mkurugenzi alishawasilisha andiko ambalo tuna makadirio ya gharama zinazohitajika kwa ajili ya ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimhakikishie, kwa sababu tayari ameshaleta kama kipaumbele na katika mwaka ujao wa fedha Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshatupa idhini ya kutenga bajeti ya vituo vya afya kila jimbo na katika Jimbo lake la Kilwa Kusini tutahakikisha tunapeleka fedha kwa ajili ya kituo hiki cha afya, ahsante. (Makofi)
MHE. OMAR ISSA KOMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni lini Serikali ilifanya tathmini kwa kuzingatia vigezo hivi sambamba na mgawanyo wa fedha za majimbo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tunashuhudia baadhi ya majimbo yakipata fedha kidogo ukizingatia kwamba vigezo alivyovieleza Mheshimiwa Waziri ni vikubwa zaidi ukilinganisha na Majimbo mengine na hata hali ya umaskini ni kubwa zaidi. Mfano mzuri ni Jimbo langu la Wingwi: Je, Serikali haioni iko haja ya kufanyia tathmini vigezo hivi, kwa kuzingatia sensa ya mwaka 2022? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, ni kwamba Serikali inafanya tathmini ya vigezo hivi mara kwa mara ili kuhakikisha kwamba vinakidhi uhitaji wa fedha za Mfuko wa Jimbo katika Majimbo yetu na pia kuona namna nzuri ya kuendelea kuboresha formula za hivi vigezo ili kuweza kutoa fedha kwa ajili ya maendeleo ya Mfuko wa Jimbo kwa ufanisi mkubwa zaidi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kufanya tathmini mara kwa mara, na mara itakapoona kuna maeneo ambayo vigezo vinahitaji kuongezwa au kupitiwa upya, basi suala hilo litafanyika.

Mheshimiwa Spika, pili, ni kweli kwamba fedha za Mfuko wa Jimbo zinatofautiana kutoka Jimbo moja na Jimbo lingine kwa kuzingatia vigezo hivi. Kama nilivyosema, asilimia 45 ya idadi ya watu katika Jimbo husika; kwa hiyo, Majimbo yenye idadi kubwa ya watu automatically yatakuwa na fedha nyingi zaidi, lakini kiwango cha umaskini kwa asilimia 20 pia na ukubwa wa eneo la kijiografia kwa asilimia 10, ahsante.
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina swali moja tu la nyongeza. Andiko la mradi liliwasilishwa tarehe 28 Desemba, 2021. Mwaka 2022 nilikumbushia kwa njia ya swali la nyongeza, nikapewa majibu kwamba mchakato unaendelea.

Mheshimiwa Spika, mwezi Julai, mwaka huu 2023 Mheshimiwa Deogratius Ndejembi, Naibu Waziri, TAMISEMI, alitembelea Jimboni kwangu, tulipomkumbushia hilo ndiyo akashauri kwamba tufanye wasilisho la kukumbusha. Kwa hiyo, wasilisho analoli-refer Mheshimiwa Waziri hapa ni la kukumbusha ambalo limewasilishwa mwezi Agosti mwaka huu 2023 na ninalo hapa, limefanya reference kwa andiko la msingi ambalo ni la mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, swali langu: Kwa kuwa hii ni ahadi ya Mheshimiwa Rais na ni ya muda mrefu: Je, Mheshimiwa Waziri sasa yuko tayari kutuambia ni lini kazi hii itaanza ili wananchi wa Mwanga waanze sasa na wao ku-¬play their party kwa kuanza kukusanya material site kama sehemu ya mchango wao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni kweli kwamba Halmashauri ya Mwanga iliwasilisha andiko awali mwaka 2021, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ilipitia na kuwarejeshea kwa ajili ya kuboresha maeneo ambayo yalihitaji maboresho zaidi. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, ahadi za viongozi wetu wa Kitaifa, ahadi za Mheshimiwa Rais ni kipaumbele chetu na ndiyo maana tayari tumeingiza kwenye mpango, tunafanya tathmini ya mwisho wa vigezo na wakati huo huo tunatafuta fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi katika Halmashauri hiyo ya Mwanga.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mwanga wawe na imani kwamba Serikali kuna hatua za mwisho za tathmini na mara fedha zikipatikana tutakwenda kuanza ujenzi wa stendi hiyo, ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Mwaka 2022 niliuliza swali hapa ndani ya Bunge nikajulishwa kwamba nilete andiko kwa ajili ya ujenzi wa Stendi ya Wilaya ya Biharamulo. Pia kwenye miradi ya kimkakati wa Mkoa wa Kagera kwenye bajeti ya mwaka huu 2023 tuliwasilisha pia. Sasa, naomba kujua ni lini ujenzi wa Stendi ya Wilaya ya Biharamulo utaanza ili wananchi wa Biharamulo waweze kupata huduma hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na Halmashauri ya Biharamulo kwa kuwasilisha andiko la maombi ya Mradi wa Ujenzi wa Stendi ya Halmashauri na nimwambie tu kwamba baada ya mawasilisho hayo Serikali inaendelea kupitia maandiko yale kufanya tathmini ya vigezo. Pia sambamba na hilo, kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mradi huo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba, mara fedha zikishapatikana na baada ya kupitia andiko hilo na kujiridhisha na vigezo, fedha itatafutwa kwa ajili ya kujenga stendi hiyo ya Biharamulo, ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, mwaka jana 2022 niliuliza swali na Mheshimiwa Naibu Waziri alinijibu kwa kutushauri kwamba tuandike andiko na tuwasilishe katika TAMISEMI kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Mabasi Wilaya ya Namtumbo: Je, Serikali nayo iko tayari au inaweza kutueleza ni lini nasi tutapata fedha kwa ajili ya kujenga stendi hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nimhakikishie Mheshimiwa Vita Kawawa kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha. Nafahamu Jimbo la Namtumbo na majimbo mengine yote kwa Waheshimiwa Wabunge, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa awamu, pia kupitia maandiko hayo ili baada ya hapo tuanze ujenzi wa vituo vya mabasi kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha Wakurugenzi wa Halmashauri kwamba pamoja na Serikali Kuu kutafuta fedha, lakini fedha za Serikali ni pamoja na fedha za mapato ya ndani. Kwa hiyo, ni wajibu wao kuanza kutenga fedha angalau kwa awamu, kujenga kila mwaka wa fedha wakati Serikali Kuu inatafuta fedha kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa stendi hizo, ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa jengo la Halmashauri ya Busokelo ukizingatia mpaka sasa ni miaka 10 imepita? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Serikali imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya utawala katika halmashauri zetu. Nawapongeza Halmashauri ya Busokelo kwa kupokea fedha za Serikali Kuu, lakini jengo halijakamilika kama Mheshimiwa Mbunge anavyosema. Naomba nilichukue hilo nilifanyie kazi tuweze kuona kiasi gani cha fedha hakijapelekwa kwa ajili ya ukamilishaji na tuweze kuweka mpango kazi kuhakikisha kwamba sasa fedha hiyo inapatikana lakini jengo hilo linakamilishwa kwa ajili ya kuhudumia wananchi wa Busokelo, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nina swali moja la nyongeza, lengo la kugawa maeneo ya utawala ni kurahisisha huduma kwa wananchi, lakini hapa nchini kuna Majimbo mengi sana makubwa ikiwemo Jimbo la Mbeya Mjini, Tandahimba na sehemu nyingine; je, Serikali ina mkakati gani wa kuyagawa Majimbo hayo ili huduma kwa wananchi ziwe rahisi? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tunza Malapo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba lengo la kugawa maeneo mapya ya utawala yakiwemo majimbo ni kusogeza huduma za kijamii karibu zaidi na wananchi na Serikali inatambua uhitaji wa maeneo haya. Kwa hivyo kwa utaratibu uliopo, kwa mujibu wa mwongozo lakini na sheria, mamlaka husika wanatakiwa kufuata utaratibu huo kwa maana ya Vikao Ngazi ya Vijiji, Baraza la Madiwani, DCC, RCC na kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI na pale ambapo Serikali itaona inafaa kugawa maeneo hayo ya utawala mapya basi taratibu zitafuata na maeneo hayo yatagawiwa katika utaratibu ulipo, ahsante.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, kwa kuwa imefanyika sensa hapa hivi karibuni na ziko kata zimeonekana ni kubwa zaidi zinahitaji mgawanyo pamoja na tarafa ikiwemo Kata ya Mandewa na Kata ya Minga. Nataka kujua mkakati wa Serikali ni nini kifanyike sasa ili kuweza kuzigawa kata hizo na kusogeza huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Mussa Sima, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tunafahamu kwamba kuna kata kubwa, kuna tarafa kubwa na Serikali inatambua inatambua umuhimu wa kugawa maeneo hayo kusogeza huduma za kijamii, lakini utaratibu ni uleule tuanze kwenye Vikao vya Kisheria katika ngazi zetu za Vijiji, Kata, Wilaya, Mkoa kisha kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya kufanya tathimini ya vigezo hivyo na kuona uwezekano wa kupata maeneo hayo, ahsante. (Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ukiona mchakato uliopo sasa hivi kufikia uamuzi huo ni mrefu sana. Kwa nini Serikali isiachie jukumu hilo katika level ya juu (Serikali Kuu) ndiyo ifanye maamuzi badala ya vikao vyote hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, utaratibu huu umewekwa kwa sababu kugawa maeneo ya kiutawala pia kuna hitaji ridhaa ya wananchi kutoka katika maeneo husika. Serikali hii sikivu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali ya Awamu ya Sita, lakini hata Serikali zilizopita zinahitaji kuwashirikisha wananchi katika kugawa maeneo yao ya utawala ndiyo maana mfumo huu ni muhimu na vizuri sana utaratibu huu ukafuatwa, ahsante. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kama alivyosema Mheshimiwa Kajege Sensa ya Watu na Makazi mojawapo ya jambo la kutusaidia ni kupanga Mipango ya Maendeleo.

Je, Serikali haioni kwamba kwa kutumia Taarifa na Takwimu za Sensa ya Watu na Makazi ikaona kabisa kuna maeneo yanahitaji kufanya mgawanyo then yenyewe ikashusha kwetu sisi wananchi na sisi tukasema ndiyo au hapana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato David Mchumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, taratibu ambazo zimewekwa kwa mujibu wa sheria ni sheria ambazo sisi kama Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tulizitunga na lengo la sheria hizi kama nilivyotangulia kusema ni kuhakikisha kwamba tunawashirikisha wananchi katika kuamua mipaka, lakini pia kupata maeneo ya utawala.

Kwa hiyo nafikiri utaratibu huu ambao upo ni muhimu ufuatwe, lakini kama kuna maoni zaidi ya kuona ni namna gani tunaweza tukaboresha basi Serikali iko tayari kusikiliza maoni na kuyafanyia kazi, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna majibu mengine yanasikitisha sana. Kituo cha Mugeta kimeisha mwaka 2019, wakati kituo hiki tunajenga tulipewa shilingi milioni 700, siyo kwamba hela zinatafutwa hapana, shilingi milioni 700, shilingi milioni 400 wakasema tujenge majengo kwa kushirikiana na wananchi na shilingi milioni 300 zinaenda MSD vifaatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulipoenda kufuatilia mwaka 2020 tukaambiwa vifaatiba vitakuja vya shilingi milioni 161 na vimeshakuja. Wakasema vifaa vingine vya shilingi milioni 139 viko njiani, leo unaambiwa kuna bajeti inatengwa, hizi shilingi milioni 300 zilizoenda MSD ziko wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kujua tutatengaje bajeti ambayo tayari ilishaenda? Kwa hiyo, naomba hili jokofu la Mugeta lipelekwe, fedha zipo MSD. (Makofi)
Swali la pili, tumejenga Kituo cha Afya Hunyari lakini hakina theater, sasa naomba kujua ni lini hii theater ya Kituo cha Afya Hunyari itakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namwelewesha Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha za vifaatiba haimaanishi ni fedha za kununua jokofu la mochwari peke yeke. Tukikamilisha ujenzi wa kituo cha afya vifaatiba vya kipaumbele ni vifaa ambavyo vitakwenda kutibu wananchi. Vifaa vya upasuaji, vifaa vya wodini, vitanda, magodoro na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua ya pili tunakwenda kupeleka vifaa kwa ajili ya kuhifadhia maiti kwa maana ya majengo ya mochwari pamoja na majokofu. Kwa hiyo, hiyo shilingi milioni 300 ambayo ilikwenda MSD ilinunua vifaatiba ambavyo viliwezesha kituo cha afya hicho kuanza kutoa huduma kwa wananchi. Mwaka huu wa fedha tayari Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameshawaletea shilingi milioni 700 kwa ajili ya kununua vifaatiba vingine likiwemo jokofu la mochwari. Naomba Mheshimiwa Mbunge tuishukuru Serikali kwamba imefanya kazi kubwa, imeleta fedha nyingi za vifaatiba, jokofu litanunuliwa kati ya Februari na Machi ili wananchi wa Bunda waweze kupata huduma nzuri za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kuhusu Kituo cha Afya cha Hunyari ni kweli kwamba kuna majengo ambayo yamejengwa lakini bado hatuna jengo la upasuaji. Safari ni hatua, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa awamu ili twende kukamilisha majengo mengine kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Hunyari. Ahsante. (Makofi)
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza naishukuru Serikali kwa kutupatia gari la ambulance katika Kituo cha Afya cha Kinesi. Kituo cha Afya cha Kinesi kinahudumia tarafa mbili kwa maana ya vijiji zaidi ya 25. Kwa sasa tunapopata maafa Wananchi hutulazimu kusafirisha miili ya ndugu zetu hawa kwenda Musoma Mjini kwa kutumia mtumbwi ama boti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tayari tuna jengo la mochwari katika kituo hiki, ni nini mpango wa dharura kuhakikisha kwamba mnatupatia jokofu ili kunusuru na kuondoa adha wanayopata Wananchi wakati wanapopata maafa haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Serikali ilipeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kinesi, kimekamilika na kinatoa huduma. Tunafahamu kwamba kituo hiki bado hakijakamilisha ujenzi wa jengo la kuhifadhia maiti na upo katika hatua ya asilimia 85. Tunafahamu pia kwamba jengo hili halijapata mashine kwa maana ya jokofu la kuhifadhia miili ya marehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuchukua fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Rorya kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambaye alishatoa maelekezo hayo, kwamba wahakikishe kupitia mapato ya ndani wanakamilisha asilimia 15 iliyobaki kukamilisha jengo la mochwari. Mheshimiwa Rais ameshapeleka shilingi milioni 400 kwa ajili ya kununua vifaatiba na kati ya fedha hiyo watenge hiyo shilingi milioni 32.5 kwa ajili ya kununua jokofu la kuhifadhia maiti kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kinesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema kwa ujumla, tumekuwa na hoja nyingi za Waheshimiwa Wabunge kutoka katika Majimbo yote, Mheshimiwa Rais amepeleka fedha shilingi milioni 500, vituo vya afya vimekamilika vimeanza kutoa huduma. Wakurugenzi wa Halmashauri, Waheshimiwa Wakuu wa Wilaya wasimamie mapato ya ndani kukamilisha majengo ya kuhifadhia maiti katika vituo vyote ambavyo vimekamilika ili kuondoa kero hiyo kwa wananchi. Kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshaleta fedha ni kazi ndogo ya shilingi milioni 30 tu kukamilisha yale majengo lakini pia waweke kipaumbele kununua majokofu kwa ajili ya majengo hayo katika vituo hivyo. Ahsante.(Makofi)
MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo lililopo kwa Getere na mimi liko kwangu Mwibara; je, ni lini Serikali itajenga majokofu katika Vituo vya Afya vya Kasaunga, Kisolya, Kasuguti na Isanju?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Kajege, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeshaelekeza Halmashauri zetu zote kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya kukamilisha majengo ya mochwari, pia kutenga fedha ambazo zinapelekwa kwa ajili ya vifaatiba kwa ajili ya kununua majokofu ya mochwari. Kwa hiyo, nakuhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia kuona Halmashauri ya Rorya Jimbo la Mwibara pia wanatenga na kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma zinazostahili. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wananchi wa Kijiji cha Lungemba na Kitelewasi kwa kushirikiana na Halmashauri na Mfuko wa Jimbo wamejenga majengo ya mama na mtoto; je, Serikali iko tayari kuwasapoti kwa kuwaletea vifaatiba katika majengo hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nawapongeza Wananchi wa Lungemba na Kitelewasi kwa kuchangia nguvu zao kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya huduma ya mama, baba na mtoto. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba vituo vyote ambavyo vimejengwa kwa nguvu za wananchi vikishasajiliwa Serikali inachangia nguvu zake, kwa maana ya kupeleka fedha kuhakikisha kwamba vinaanza kutoa huduma. Kwa hiyo, tuko tayari kuwaunga mkono wananchi kwa ajili ya kuanza kutoa huduma katika majengo haya, ahsante.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Tunaishukuru sana Serikali kwa kutupatia gari la wagonjwa ambalo tumelipeleka katika Kituo cha Afya cha Umbwe. Kituo hiki cha afya kinahudumia Kata sita katika Tarafa ya Kibosho na hakina mortuary. Je, Serikali ina mpango gani wa kutusaidia kutujengea mortuary katika kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Profesa Ndakidemi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza natumia fursa hii kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge na kuwapongeza kwa kupokea magari ya wagonjwa ambayo Mheshimiwa Rais amenunua kwa ajili ya Majimbo yetu na Halmashauri zetu zote kote nchini. Pamoja na hilo tunaendelea kuboresha sana huduma za mortuary, natumia nafasi hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Moshi Vijijini kutenga fedha ya mapato ya ndani kwa ajili ya jengo la mortuary na kutumia fedha ya vifaatiba kwa ajili ya kununua majokofu ili kuboresha huduma kwa wananchi, ahsante. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kiponzero ni moja ya vituo kongwe katika Jimbo la Kalenga, bahati mbaya mpaka leo hakina cha chumba cha mortuary; je, ni lini Serikali itatupa jokofu pamoja na chumba cha mortuary?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Jackson Kiswaga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza na narejea kusema kwamba maelekezo yameshatolewa kuhakikisha kwamba Wakurugenzi wanajenga majengo ya kuhifadhia maiti. Pia wananunua majokofu katika vituo vyote vilivyopo ambavyo vinatoa huduma kote nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, namuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Iringa Vijijini kuhakikisha wanaanza kujenga jengo la mortuary, lakini pia wananunua jokofu kwa ajili ya Kituo cha Afya cha Kiponzero, ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa naishukuru Serikali kwa ujenzi wa Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali kwenye Mkoa wetu wa Morogoro. Hii Zahanati ya Uwanja wa Ndege ina upungufu wa wafanyakazi hasa manesi na madaktari. Je, ni lini mtapeleka hao Manesi na Madaktari ili kutimiza ikama? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, Kituo cha Afya Mafiga kimekuwa na tatizo sana la theatre na wanawake wengi wajawazito wanapenda sana kujifungulia pale, na mara wanapopata matatizo, wanapelekwa Hospitali Kubwa ambapo kuna mwendo. Je, ni lini Kituo hiki cha theatre kitajengwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Zahanati hii ya Uwanja wa Ndege ina watumishi watano; Afisa Tabibu mmoja, Wauguzi wawili, Mtaalamu wa Maabara mmoja na Mhudumu wa Afya mmoja. Kwa idadi ya wananchi ambao wanatibiwa pale, tunahitaji kuongeza wataalamu. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, tayari Serikali imeshaitambua Zahanati hiyo, mara ajira zitakapojitokeza, tutahakikisha tunawapa kipaumbele kwa ajili ya kuongeza idadi ya watumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu swali la pili, Kituo cha Afya cha Mafiga ni kweli kipo mjini na kinahudumia wananchi wengi na kina upungufu wa baadhi ya miundombinu ikiwepo majengo ya upasuaji na majengo mengine. Tushamwelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Morogoro kuandaa mchoro wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Mafiga. Nitumie fursa hii kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafuatilia ili tuweze kuona umefikia hatua gani na tuone uwezekano wa kuongeza majengo katika Kituo cha Afya cha Mafiga, ahsante. (Makofi)
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri; je, ni lini Serikali itaongeza fedha za ujenzi wa Zahanati kwenye vijiji hasa Majimbo ya Vijijini? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gulamali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikijenga Vituo vya Afya katika maeneo ya vijijini kwa kuchangia nguvu za wananchi kwa kutoa shilingi milioni 50 kwa ajili ya umaliziaji. Fedha hiyo shilingi milioni 50 ilianza kutolewa mwaka 2016/2017 na ukizingatia kasi ya inflation kwa sasa, tumeshapitia bajeti za ujenzi wa Vituo vya Afya, Zahanati na pia Hospitali za Wilaya. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari Serikali imeshafanya kazi hiyo ya kubadili au kuongeza kiasi cha fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati. Taarifa rasmi itatolewa na Waheshimiwa Wabunge mtaipata na fedha zinazokuja zitakuwa na mabadiliko ili kuendana na inflation iliyojitokeza, ahsante. (Makofi)
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Baadhi ya zahanati ambazo zimejengwa Makao Makuu ya Kata hasa Sirop, Dirma, Laghanga, Getanuwas na Ishponga hazina jengo la mama na mtoto; je, Serikali ina kauli gani ili kuboresha afya ya mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Samweli Hhayuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati zote ambazo zimejengwa na zina upungufu wa majengo ya Huduma za Afya ya Mama, Baba na Mtoto, tumeshatoa ramani nyingine kwa ajili ya kuongeza majengo hayo kwenye zahanati hizo ili huduma hizi ziweke kupatikana. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba zahanati ambazo amezitaja hapa tutazipa kipaumbele pia kuhakikisha kwamba zinajenga majengo hayo, ahsante.
MHE. YUSTINA A. RAHHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nami naomba kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Zahanati ya Nahasey Wilayani Mbulu ambayo iko katika mazingira magumu hasa sehemu ya mama na mtoto na kutoa huduma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, zahanati hizi ambazo zinaendelea kujengwa katika maeneo yetu, zinatumia fedha za mapato ya ndani na pia fedha kutoka Serikali Kuu. Kwa hiyo, naichukua hoja ya Mheshimiwa Mbunge na baada ya hapa tutafuatilia kule Bunda tuone chanzo cha fedha ambacho kinaweza kupatikana mapema iwezekanavyo ili tuweze kukamilisha ujenzi wa zahanati hii yakiwemo hayo majengo ya Huduma ya Afya ya Mama, Baba na Mtoto, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama yote hayo wanayafahamu, sasa ni zaidi ya mwaka wa tatu tumesimama hapa kuomba Kituo cha Afya cha Ngerengere, hakina jengo la Huduma ya Mama na Mtoto, Mortuary hakuna. Wakazi wa Kata ya Ngerengere ni 15,000, Kata ya jirani ya Kidugalo ni 8,000, leo hii Mheshimiwa Waziri anajibu majibu ambayo anafahamu tatizo liko wapi, mpaka nashindwa kuelewa. Naomba kumwuliza swali Mheshimiwa Waziri; je, ni lini mtakwenda kutatua hili tatizo? Siyo kwamba majibu mnayo na utatuzi hakuna, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hamisi Shabani Taletale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wa upanuzi wa Kituo cha Afya cha Ngerengere. Nasi kama Serikali, taarifa hii tunaifahamu na ndiyo maana tulitoa maelekezo kwa Mkurugenzi, kuongeza eneo la ujenzi wa Kituo cha Afya, ekari 4 na nusu hazitoshi kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya hiki kilikuwa ni cha Mission, kwa hiyo, kilichukuliwa na Serikali kikiwa tayari kinatoka Mission. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba mara hili eneo la ekari mbili la Posta ambalo halijaendelezwa, ambalo liko mkabala kabisa na Kituo hiki, likishachukuliwa na kuwa na ekari sita na nusu, basi mapema iwezekanavyo tutatafuta fedha kwa ajili ya kuongeza majengo haya ambayo yanapungua katika Kituo cha Afya cha Ngerengere, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Kata ya Mbande ya Chamazi katika Mkoa wa Dar es Salaam ni kata ambayo ina idadi kubwa ya watu, lakini wana Zahanati ya Mbande: Ni lini sasa Serikali itaipandisha Zahanati ya Mbande kuwa Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Mariam Kisangi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba idadi ya wananchi katika Kata ya Mbande kule Chamazi ni kubwa na Zahanati ile ya Mbande kwa kweli inazidiwa na idadi ya wananchi na sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI tumeshaainisha kwamba eneo la Zahanati ya Mbande ni sehemu ya eneo la kimkakati kuona uwezekano wa kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hilo tunalifanyia kazi na tutahakikisha kwamba tunatafuta eneo linalotosheleza kama lile la Zahanati linatosha ama tunahitaji kupata eneo lingine kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya kwa manufaa ya wananchi walio wengi katika eneo lile, ahsante. (Makofi)
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa mwenyekiti, wananchi wa Kata ya Kabwe wana changamoto ya kijiografia na wanapata shida kubwa sana ya matibabu kuja Hospitali ya Wilaya; na ile ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kujengewa Kituo cha Afya. Ni lini mtapeleka fedha kumalizia kujenga kituo hicho ili wananchi wapate huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi zinazotolewa na viongozi wetu wa Kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji. Kwa sababu hii ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, na ninakumbuka nilikuwa kwenye ziara yake, nakuhakikishia tayari tumeshaingiza kwenye Mpango Mkakati kwa ajili ya kutafuta fedha na kwenda kujenga Kituo cha Afya katika Kata ya Kabwe, ahsante. (Makofi)
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, kwa kuwa Tarafa ya Ndagalu Kata ya Ng’haya, Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu ilitoa fedha kwa ajili ya kuweka miundombinu kwenye Zahanati ya Ng’haya ili kuipandisha hadhi kuwa Kituo cha Afya.

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu ya zahanati hiyo kuwa Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, natumia nafasi hii kumsisitiza na kumkumbusha Mkurugenzi wa Halmashauri ya Magu, kwamba tulishawaelekeza kwanza kufanya tathmini ya majengo yanayopungua kwenye ile zahanati ili iwe na hadhi ya kupandishwa kuwa Kituo cha Afya. Kwa hiyo, nitafuatilia Mheshimiwa Kiswaga, tuweze kuona wamefikia hatua gani kwa maana ya Mkurugenzi na timu yake, pia tuone namna gani tunapata fedha, iwe ni kwa mapato ya ndani ya Halmashauri au kwa fedha kutoka Serikali Kuu ili tuweze kupandisha hadhi hii Zahanati ya Ng’haya iweze kuwa Kituo cha Afya, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mwaka 2021 Kata ya Mgombezi kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini walipatiwa shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya. Baadhi ya majengo yalijengwa lakini mpaka sasa tunapoongea, shilingi milioni 250 za ziada hazijafika kwenye ile Kata ya Mgombezi, zaidi ya miaka miwili. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, ni lini Serikali itatuletea shilingi milioni 250 zilizobaki ili kwenda kumalizia Kituo cha Afya cha Mgombezi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna Vituo vya Afya katika Majimbo mengi hapa nchini ambavyo vilipewa shilingi milioni 250 mwaka wa fedha 2021/2022 na majengo ya shilingi milioni 250 yamekamilika, yameanza huduma za awali za OPD kwenye baadhi ya Vituo lakini kuna majengo yanayohitajika kwa ajili ya kukamilisha ngazi ya Kituo cha Afya. Naomba kumhakikishie Mheshimiwa Kimea kwamba tunatambua Vituo vyote ambavyo vimepata shilingi milioni 250 na bado shilingi milioni 250.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametupa kibali kuweka kwenye bajeti ambayo tunaanza kuipanga hivi karibuni, kuhakikisha Vituo vyote vya Afya vilivyopata shilingi 250 na bado shilingi milioni 250, vinapelekewa mwaka ujao wa fedha ili vituo vile viweze kukamilika, ahsante. (Makofi)
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana; Mji wa Mafinga ni Mji ambao unakuwa kwa kasi kubwa sana. Kuna Kituo cha Afya cha Upendo ambacho wananchi walishaanza kukijenga. Ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Kituo hicho?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Tendega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inathamini nguvu za wananchi na tutakwenda kufanya tathmini ili tuone namna gani tunachangia kukamilisha Kituo cha Afya cha Upendo. Ahsante. (Makofi)
MHE. MUNDE T. ABDALLAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante; nimekuwa nikiuliza kila siku kuhusu Zahanati ya Town Clinic ambayo ina msongamano mkubwa wa watu kufikia kuzalisha wanawake 200 kwa mwezi, na Mheshimiwa Naibu Waziri amekuwa akinijibu Mkurugenzi alete michoro; je, Mheshimiwa Naibu Waziri ana mkakati gani wa kumwandikia sasa Mkurugenzi kwa maandishi ili aweze kuleta huo mchoro na Zahanati ya Town Clinic iwe Kituo cha Afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Munde, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Munde, alikuja, tulimwita Mkurugenzi wa Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, tulikaa naye mimi, Mheshimiwa Mbunge na Mkurugenzi, tukampa mkakati wa kwenda kuandaa michoro hiyo aweze kuiwasilisha. Si kwa barua, bali tulimwita na tukakutana. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tuna taarifa zote za hatua ambazo zinaendelea kwa ajili ya kupandisha hadhi Zahanati ile ya Town kuwa Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasisitiza kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Tabora kuleta michoro ile haraka iwezekanavyo Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona namna gani tunaanza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Town. Ahsante. (Makofi
MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, namuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, Zahanati ya Kijiji cha Nkome nimekizungumza humu mara tatu; inazalisha shule kila mwezi, maana yake watoto zaidi ya 550; na kwa sasa tumeenda zaidi tunafika karibia 600 kwa mwezi; mliniahidi kuongeza uwezo wa ile zahanati ili iwe Kituo cha Afya, tathmini zote zimefanyika na mwezi huu wametoka kukagua tena, na fedha ipo shilingi milioni 500; lini hiyo fedha itakuja? Lini Mheshimiwa Naibu Waziri atakuja ili akaangalie huo uzalishaji wa hiyo zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Musukuma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Zahanati hii ya Nkome aliyoitaja Mheshimiwa Mbunge, kwa kweli imezidiwa kwa idadi kubwa ya wananchi katika eneo lile na Serikali ishaweka mpango wa kupandisha hadhi kuwa Kituo cha Afya. Mwenyewe amesema wiki moja, mbili zilizopita wataalamu kutoka Ofisi ya Rais, TAMISEMI, walifika kufanya tathmini kwa ajili ya kutumia fedha za Benki ya Dunia kujenga Kituo cha Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili liko on track na tutahakikisha tunajenga Kituo cha Afya hiki mapema iwezekanavyo. Ahsante. (Makofi)
MHE. CHARLES JOHN P. MWIJAGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nisikitike kwa majibu ya Serikali. Serikali imegawa ambulance lakini sisi Wilaya ya Muleba ambayo 70% ni maji na kuna visiwa 38 hatuna kifaa sio dharura yaani ndiyo maisha yetu visiwa 38 vinahitaji vesal realiable vesal ya ku-move. Serikali hamuoni kwamba mchukue jitihada za Mheshimiwa Rais ku-copy ile vesal mliyopeleka Mafia na sisi mtununulie kama hiyo kusudi wananchi waweze kufika katika sehemu za huduma kwa sababu eneo hilo lina watu wengi.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba tu nimuhakikishie Mheshimiwa Mwijage kwamba Serikali ya awamu ya Sita inatia kipaumbele cha hali ya juu sana katika maeneo ambayo hayafikiki kuhakikisha kwamba huduma za rufaa zinatekelezwa ipasavyo. Ndiyo maana sasa imeandaa mpango makakati wa kuainisha maeneo yote ambayo ni magumu kufikika yale ambayo yanahitaji boat ambulance ikiwemo Halmashauri ya Muleba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie kwamba tayari tupo hatua nzuri na mwaka ujao wa Fedha 2024/2025 tunaanza kutenga fedha kwa ajili ya kupata hizo boat ambulance.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na nia hii ya kugawa kata tuna nia pia ya kugawa vijiji na mwaka unaokuja ni mwaka wa uchaguzi. Je, Serikali inatoa kauli gani kwa Halmasahuri ya Wilaya ya Mbinga ambayo vijiji vingi vimeleta maombi ya kugawanywa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kauli ya Serikali ni kwamba taratibu za kisheria za maombi ziendelee, na Serikali itapokea maombi hayo kupitia Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, itafanya tathimini ya vigezo lakini kipaumbele cha kwanza kwa sasa ni kuboresha kwanza maeneo ya kiutawala yaliyopo. Lakini hili halizuii kuendelea na taratibu katika ngazi ya halmasahuri, ahsante. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kupata majibu ya Serikali. Nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali kwa kipindi hiki imesimamisha utoaji wa mikopo ili kupisha kuandaa utaratibu mzuri wa utoaji mikopo hiyo.

Je, Serikali haioni haja kuwa na mpango wa dharura wa kutoa mikopo wakati tunasuburi utaratibu huo mpya kwa sababu wananchi wnahitaji sana mikopo hiyo hasa kipindi hichi cha kilimo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, lengo la Serikali kusitisha utoaji wa mikopo hii ilikuwa ni kuhakikisha kwamba fedha zinazotengwa kwa ajili ya mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu zinawafikia walengwa lakini pia zinatumika kwa tija na kurejeshwa ipasavyo. Hiyo ndiyo ilikuwa changamoto kubwa iliyopelekea kusitisha utoaji wa mikopo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendanalo hili jambo kwa kasi ili mapema iwezekanavyo utaratibu rasmi uwezekutolewa na mikopo ianze kutolewa kwa wananchi badala ya kuwa na utaratibu wa dharura ambao utakuwa hauna tija sana kwa sababu bado utakuwa na mapengo mengi. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba si muda mrefu sana Serikali itatoa utaratibu na mikopo ya 10% itaanza kutolewa kwa wananchi wetu, ahsante. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Naomba kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Lindi una maeneo mengi sana yaliyoko mbali na hospitali za Wilaya yakiwepo Kilimarondo kule Nachingwea, Nanjilinji Kilwa, Milola kule Mchinga; je, Serikali itatupa kipaumbele kutupatia magari hayo yaliyoongezwa katika maeneo hayo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tecla Mohamed Ungele, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, magari haya yatakayoletwa kuna halmashauri zitapata magari zaidi ya moja. Sababu ya halmashauri hizo kupata magari zaidi ya moja itakuwa ni kukidhi vigezo vya kitaalamu, ikiwemo umbali kutoka kituo hicho kwenda kituo kingine cha jirani, lakini pia population ya eneo hilo pamoja na mazingira ya kijiografia. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Ungele kwamba, tutafanya tathmini kwa Halmashauri hizo alizozitaja ili kuona kama zinakidhi vigezo hivyo. Ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Hospitali ya Mkoa wa Simiyu muda mrefu hatuna gari la kukusanya damu salama; je, ni lini Serikali itatununulia gari la kukusanya damu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, magari katika hospitali za rufaa za mikoa yanaratibiwa na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, lakini kwa kushirikiana kwa karibu na Wizara ya Afya. Kwa hiyo, kwa sababu hospitali hii iko chini ya Wizara ya Afya tutawasiliana na Wizara ya Afya ili tuone uwezekano wa kupata gari hilo kwa ajili ya huduma za damu. Ahsante.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Naomba niulize swali la nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka magari ya wagonjwa katika Jimbo la Mbulu Mji na Mbulu Vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, magari mawili yatanunuliwa na kupelekwa Halmashauri ya Mbulu Mjini na Mbulu Vijijini. Ahsante.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na mimi kunipa nafasi niulize swali la nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na uhitaji mkubwa wa gari la wagonjwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Liwale lakini tunayo shida kubwa ya magari ya chanjo. Watoto sasahivi ni miaka miwili hawapati chanjo kwa sababu ya ukosefu wa gari; je, Serikali haioni umuhimu wa kutupatia gari kwa ajili ya chanjo za watoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Jimbo la Liwale, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mbali na magari 195 ya wagonjwa Serikali itanunua magari mengine 204 kwa ajili ya shughuli za usimamizi, lakini pia shughuli za chanjo. Kwa hiyo pamoja na halmashauri zote kupata magari ya wagonjwa kutakuwa na gari jingine ambalo litakuwa kwa ajili ya shughuli za usimamizi na shughuli za chanjo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Kuchauka kwamba, gari hilo pia litakuja sambamba na gari la wagonjwa.
MHE. AGNES E. HOKORORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Likombe kilichopo Mtwara ndicho pia kinatumika kama hospitali ya Wilaya kwa sababu katika Wilaya hiyo hakuna hpspitali ya Wilaya;

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la wagonjwa kwa sababu kuna wagonjwa wengi hasa akinamama wanaotaka kujifungua?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hokororo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba, Kituo cha Afya cha Likombe kina-serve kama hospitali ya halmashauri kwa sababu hatuna hospitali ya manispaa. Hata hivyo, nimhakikishie kwamba Manispaa ya Mtwara ni moja ya halmashauri zitakazopata gari la wagonjwa. Kwa hiyo nimuelekeze mkurugenzi kuhakikisha unazingatia vigezo ikiwezekana wapeleke gari hili katika kituo hiki kwa kadiri ya vigezo ambavyo vimewekwa na Serikali. ahsante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, nina swali moja la nyongeza.

Je, wakati huo ambao taratibu za kujenga kingo zinaendelea, Serikali haioni haja ya kutoa fedha angalau Shilingi milioni 100 kwa ajili ya kusafisha Mto Kanoni ili kupunguza athari zake hususan Kata nne ambazo zinaathirika zaidi; Kata ya Bilele, Bakoba, Hamugembe na Nshambya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Oliver Semuguruka kwa kadri anavyowakilisha wananchi wa Mkoa wa Kagera, lakini pia, anavyowasemea ipasavyo wananchi wa Mkoa huo. Vile vile nampongeza sana Mheshimiwa Stephen Byabato, Mbunge wa Jimbo la Bukoba Mjini anavyowasemea na kuwawakilisha ipasavyo wananchi wa Bukoba na anavyoshirikiana na Waheshimiwa Wabunge wa Viti Maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitambue kwamba wapo Waheshimiwa Madiwani, Mstahiki Meya na Mkurugenzi wa Bukoba Manispaa. Nitoe maelekezo kwa Mkurugenzi kuhakikisha wakati tunasubiri mradi huu wa ujenzi wa kingo kwa maana ya mradi wa TACTIC, watenge fedha kwa kadri inavyowezekana kuendelea kuboresha kingo na kina za Mto Kanoni ili kuzuia madhara hayo wakati bajeti hiyo inakuja kutekelezwa, ahsante. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa Kata ya Masama Kati tayari tulishatenga eneo kwa maana ya Kituo cha Afya chenye hadhi ya Kituo cha Afya na wewe mwenyewe umeshafika pale, na tayari tumeshatenga fedha ya kujenga OPD: Je, ni lini Serikali itatuletea fedha ya kumalizia majengo hayo yaliyobaki ambayo pia ni ahadi yako kama sehemu ya Serikali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nipokee ombi la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe. Nafahamu tulishafanya ziara kule pia, tukaenda kwa Nsila, tumeanza ujenzi wa Kituo cha Afya kwa Shilingi milioni 250, nafikiri zinaongezeka nyingine. Hicho tutaenda kukifanyia tathmini kuona kama kinakidhi vigezo vya kujenga Kituo cha Afya tuweze kupeleka fedha kwa awamu, ahsante. (Makofi)
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niulize swali langu la nyongeza, kwamba kwa kuwa Kituo cha Afya cha Kazuramimba ni kata ya kimkakati. Sasa ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kujenga majengo mengine? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bidyanguze, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwakikishie kwamba Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan tayari imeshaainisha maeneo yote ya kata za kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwa awamu na mpaka sasa imeshajenga vituo vyake 466 vyenye thamani ya shilingi bilioni 718 na Kituo cha Afya cha Kazuramimba ni miongoni mwa vituo hivyo ambavyo vitatengewa fedha kwa ajili ya majengo mengine, ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi pamoja na jitihada hizo nzuri za Serikali lakini vituo vingi vya afya ikiwemo cha Bumilainga na Ifingo bado havijakuwa na miundombinu ya kutosha ikiwemo kuwepo wodi ya akinamama na wodi ya wanaume.

Je, Serikali iko tayari kwenda awamu ya pili kwa kuanza kujenga facilities hizo muhimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Jimbo la Mafinga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwakikishie tu kwamba Serikali iko tayari kuendelea na ujenzi wa majengo ya wodi za wanawake na wanaume katika Kituo cha Afya cha Ifingo na kituo hicho alichokitaja pia katika vituo vyote ambavyo vimejengwa awamu ya kwanza vyote vitakwenda awamu ya pili kwa ajili ya kukamilisha miundombinu, ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nifanye marekebisho kidogo, siyo Halmashauri ya Mji wa Tukuyu ni Mji wa Tukuyu, kwa mujibu wa taratibu na sheria nataka nijue majukumu hasa miji midogo ni nini? Wale watumishi wa miji midogo wanatakiwa wafanye majukumu gani hasa katika ukusanyaji wa mapato ya ndani pamoja na matumizi yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niiombe Serikali kama ingeweza ikaandaa mwongozo ambao utasaidia hii miji midogo kuweza kujitegemea na kukua ili hatimaye baadae wawe na uwezo kuwahudumia wananchi katika maeneo yao ya kiutawala hasa katika ukusanyaji wa mapato na matumizi na kuyasimamia matumizi hayo, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka za miji midogo zilianzishwa kwa mujibu wa sheria na zina majukumu yake na zina Baraza la Madiwani wa Mamlaka ya Mji Mdogo. Pia zina mtendaji wa mamlaka lakini pia zina mwenyekiti wa mamlaka ya mji mdogo. Kazi zao pamoja na majukumu mengine ni pamoja na kuhakikisha kwamba zinakusanya mapato katika eneo lao la utawala katika mitaa yao. Pia kuwasilisha mapato hayo katika account ya halmashauri mama ambapo mkurugenzi wa halmashauri ndiye accounting officer wa halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kusimamia miradi ya maendeleo ambayo inatekelezwa katika mitaa ambayo inaunda mamlaka ya mji mdogo, Mamlaka ya Mji Mdogo ni hatua ya kwanza ya kuelekea kupata kibali au kupandishwa hadhi kuwa Halmashauri ya Mji. Kwa hiyo, hii ni hatua ya mwanzo wakati wanajenga uwezo wao kujiendesha kuelekea kwenye Halmashauri ya Mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swala la pili; kuhusu mwongozo wa miji hii kujitegemea, kwa sababu hii ni hatua ya kukua kuelekea kwenye Halmashauri ya Mji maana yake ukishafika hatua ya Halmashauri ya Mji wanakuwa na mkurugenzi ambaye ndiye accounting officer na inakuwa ni Baraza la Madiwani la halmashauri ya mji mambalo lina majukumu yote kwa mujibu wa sheria za Serikali za Mitaa, ahsante.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana natambua kwamba kijiji ni mamlaka ya utawala, kata ni mamlaka ya utawala na halmashauri ya mji au ya wilaya au jiji ni mamlaka ya utawala. Nafahamu msimamo wa Serikali kuhusu uendeshwaji wa mamlaka za kiutawala. Sasa swali langu, jimbo siyo mamlaka ya utawala, Jimbo langu la Sikonge ili nifike kwenye tarafa ile ya mradi natembea kilometre 200, ili nifike kwenye Kata ya mbali kabisa mpakani mwa Singida natembea kilometre 400. Sasa swali langu ni kwamba kwa nini Serikali hairuhusu uanzishwaji wa majimbo mapya ili uwakilishi wa wananchi uwe mzuri zaidi hapa Bungeni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Joseph Kakunda Mbunge wa Jimbo la Sikonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli na ni sahihi kama Mheshimiwa Mbunge alivyosema kuhusiana na mamlaka za utawala katika ngazi za vijiji, kata, halmashauri na maeneo mengine. Pili, jimbo ni eneo ambalo linauwakilishi wa wananchi na yeye ndiyo Mbunge wa jimbo hilo. Namshauri kwa sababu taratibu za kuomba majimbo mapya zinafahamika nimuombe tu Mheshimiwa Mbunge afuate taratibu zile na kufikisha mahala ambapo kuna mamlaka hiyo hiyo ili waweze kuona uwezekano wa kuchukua hatua hizo kwa mujibu wa mahitaji ya jimbo lake, ahsante.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi ina zaidi ya umri wa miaka 20 na mchakato wa kuomba halmashauri ulishapita katika ngazi ya wilaya, mokoa na TAMISEMI na kwa kuwa Jimbo la Mikumi au Tarafa ya Mikumi siyo halmashauri wala siyo makao makuu ya wilaya imepitwa na fursa zote za miradi ya kimkakati. Je, nini mpango wa Serikali katika kukumbuka miji hii ambayo haina hadhi ya wilaya au halmashauri katika miradi mikubwa ya kimkakati kama TACTICs na miradi mingine?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dennis Londo Mbunge wa Jimbo la Mikumi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, uanzishwaji wa mamlaka za miji midogo ikiwemo Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi ulianzishwa kwa dhamira njema ya Serikali kuhakikisha kwamba inasogeza huduma za jamii karibu zaidi na wananchi. Hiyo ndiyo sababu ya msingi Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi ilianzishwa lakini pia na mamlaka za miji midogo maeneo mengine kote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi kwa kuwepo kazini kwa zidi ya miaka 20 lakini pia kwa kuwasilisha maombi ya kuomba kuwa Halmashauri ya Mji wa Mikumi kwa kufuata taratibu zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI tunatambua kwamba Mamlaka ya Mji Mdogo wa Mikumi ishawasilisha maombi yao na taratibu zinazoendelea sasa ni kujiridhisha na vigezo hivyo. Pale wakati utakapofika kwa ajili ya kuanzisha Halmashauri ya Mji wa Mikumi basi hatua hizo zitachukuliwa kwa manufaa ya wananchi wa Mikumi, ahsante.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuwa Hospitali yetu ya Wilaya ya Mbozi ni chakavu sana kama ambavyo Mheshimiwa Waziri alivyosema na hizi fedha ambazo zimetengwa kwa kweli ni kidogo. Sasa nataka nifahamu kwamba Serikali ina mpango gani au mkakati gani wa kudumu kuhakikisha kwamba majengo yote ya Hospitali ya Wilaya ya Mbozi yanakarabatiwa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama alivyosema Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza kwamba Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ni hospitali kongwe ni hospitali chakavu. Ndiyo maana kwa utashi na mapenzi mema ya Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan ameainisha hospitali hiyo miongoni mwa hospitali 19 nchini kote za kipaumbele kwa ajili ya kutenga fedha kuhakikisha majengo yanakarabatiwa na kuwa na hadhi ya hospitali ya halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Mheshimiwa Rais tayari ameshatenga shilingi milioni 900 katika bajeti ya mwaka huu na itapelekwa kwa ajili ya ukarabati. Tutaendelea kutenga fedha kwa awamu kuhakikisha majengo yote ya Hospitali ya Halmashauri ya Mbozi inakarabatiwa na kutoa huduma nzuri kwa wananchi wa Mbozi, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali yanayotia moyo nina maswali mawili ya nyongeza. Kituo cha Afya Mkalama ni kituo chakavu sana kinazidiwa hata hadhi na baadhi ya zahanati. Je, Serikali haioni haja sasa ya kutamka kabisa rasmi kwamba ni lini watakwenda kufanya ukarabati kwenye kituo hiki ambacho kinahudumia tarafa kubwa sana yenye watu wengi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Kituo cha Afya Kinyangiri Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi alipita pale na kutoa ahadi na akaweka na dead line kwamba mwezi wa 12 mwaka huu kitakuwa kimeshafanyiwa upanuzi na ukarabati. Mwenyekiti wa CCM ambaye ni Rais wa Jamhuri Muungano wa Tanzania akakazia ahadi hiyo juzi alivyokuja Singida. Je, Serikali haioni kwamba kuna haja sasa ya kutamka rasmi kwamba wanakwenda kufanya ukarabati kwenye kituo hiki kwa kuzingatia kauli za wakubwa wa nchi hii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Francis Isack Mtinga Mbunge wa Jimbo la Irambva Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kituo cha Afya hilki cha Mkalama ambacho ni chakavu sana Serikali imekwisha kiainisha kama nilivyotangulia kusema. Hivi sasa tuko kwenye utaratibu wa kutafuta fedha na fedha ikipatikana mapema iwezekanavyo itapelekwa Halmashauri ya Mkalama kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Mkalama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Mkalama kwamba Serikali inatambua uchakavu wa Kituo cha Afya. Inatafuta fedha na mapema iwezekanavyo fedha ikipatikana tutahakikisha kinakarabatiwa na kuwa hadhi ya kituo cha afya kama vilivyo vituo vya afya vingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusiana na Kituo cha Afya cha Kinyangiri ni kweli ni maelekezo ya Mheshimiwa Rais na Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi. Sisi Ofisi ya Rais, TAMISEMI maelekezo ya Mheshimiwa Rais ni kipaumbele na natoa kauli rasmi kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwamba tunakwenda kutekeleza ahadi ya Rais. Tunakwenda kutekeleza ahadi ya Katibu Mkuu wa Chama cha Mapinduzi mapema iwezekanavyo, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kuniona. Changamoto zilizoko Iramba Mashariki zinafanana sana na Changamoto zilizoko Arumeru Mashariki katika Sekta ya Afya. Je, ni lini Serikali itakuja kuboresha Kituo cha Afya Makida ambacho majengo yake yamekuwa magofu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue hoja ya Kituo cha Afya cha Makida ambacho ni chakavu na kinahitaji ukarabati ili tuweze kutuma wataalam wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI lakini pia Mkoa wa Arusha kufanya tathmini na kutuletea makadirio ya gharama zinazohitajika ili tutafute fedha kwa kupitia mapato ya ndani lakini mahususi kupitia Serikali Kuu ili tuweze kukarabati kituo hiki cha afya kiweze kutoa huduma vizuri, ahsante.

MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuwa Kituo cha Afya Iramba, Wilayani Serengeti ni cha muda mrefu na kimechakaa sana ni lini sasa Serikali itatenga fedha kwa ajili ya ukarabati wa kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Amsabi Mrimi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kumuelekeza Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mara na Mganga Mkuu wa Halmashauri ya Serengeti kufanya tathmini kwa maana ya gharama zinazohitajika kwa ajili ya ukarabati wa kituo hiki cha afya na kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya kufanya tathmini lakini pia kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati wa kituo hicho, ahsante.

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana Jimbo la Singida Mashariki lina kata 13 lakini tulijaliwa kupata kata moja tu ndiyo imejengewa kituo cha afya.

Je, ni lini sasa Serikali itajenga vituoa vya afya vya kata ya Misughaa na Issuna ili kuweka uwiano mzuri katika mkakati wa afya? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Miraji Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mpango wa Serikali wa kujenga vituo vya afya vya kimkakati ni endelevu. Hivi sasa Serikali imeendelea kutafuta fedha kupitia mapato ya ndani ya Serikali Kuu, kupitia mapato ya ndani ya halmashauri lakini pia wadau mbalimbali kuhakikisha yale maeneo ambayo yameainishwa kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kimkakati yanajengwa vituo hivyo. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mtaturu kwamba tutatoa kipaumbele katika kata hizi zmbazo ameziainisha iloi pia ziweze kupata vituo vya afya, ahsante.

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Je, ni lini Serikali itajenga maabara na wodi ya kina mama na Watoto katika Kituo cha Afya cha Kasuguti?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): -Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa ujenzi wa vituo vya afya ambavyo vina majengo pungufu kwa kadiri ya standard ya vituo vya afya ni mpango ambao unaendelea kutekelezwa. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kuweka mipango kwa ajili ya kutafuta fedha lakini kwa ajili ya kwenda kufanya ujenzi wa majengo hayokatika kituo hiki cha afya, ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Spika, naomba muda wako kidogo; tarehe 6 Februari, 2024 Mwananchi Digital ilimwonesha mama ambaye amehamia shuleni, ameacha majukumu yake ya kiuchumi na kijamii ili kuweza kumsaidia mtoto wake awapo shuleni.

Swali la kwanza, je, hakuna kada inayofanana na kada hii ambayo nimeiulizia ambayo kwa sasa Serikali wakati inajiandaa kuipata kada husika inaweza ikaitumia ili kuwasaidia watoto hawa wawapo shuleni?

Swali la pili, je, ni nini mkakati wa Serikali kuipata sasa hii kada husika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli miongoni mwa wanafunzi wenye ulemavu wapo wanafunzi wenye ulemavu ambao umewaathiri kwa kiasi kikubwa na kushindwa kufanya baadhi ya majukumu ambayo kimsingi wanahitaji usaidizi wa karibu zaidi. Ndiyo maana Serikali imeweka utaratibu kuwa na vyuo vya Walimu, mafunzo maalum kwa wanafunzi wenye ulemavu, ambao kwa sasa wanatumika kuwasaidia wanafunzi hao katika mazingira hayo.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunahitaji kuwa na kada maalum ambayo inaweza ikawasaidia kwa ukaribu zaidi wanafunzi wenye mahitaji makubwa ya usaidizi katika mazingira ya shule. Kwa hivyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalifanyia kazi hilo, inatambua umuhimu wao, lakini tuna mkakati wa kuhakikisha kwamba tunaendelea kuwatumia pia Maafisa Ustawi wa Jamii katika maeneo hayo pamoja na Walimu wenye mafunzo maalum ili wanafunzi wenye ulemavu waweze kupata huduma bora zaidi.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, nikiongezea hapo ni kwamba, kwa kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Waziri Mkuu inayoshughulika na masuala ya watu wenye ulemavu sambamba na Wizara ya Elimu tumekwishaanza kufanyia kazi suala hilo la kuwa na kada maalum kwa ajili ya kutoa msaada kwa watu wenye ulemavu kwenye shule.

Mheshimiwa Spika, pia ukiangalia kwa upande wa vyuo vikuu University of Dar es Salaam wamekwishaanza. Kwa sasa tuko mbioni na tumeshapata bajeti maalum ya Mfuko wa Watu wenye Ulemavu ambao utasaidia katika kutekeleza jukumu hili. Kwa hiyo Serikali ipo katika hatua nzuri.
MHE. BAHATI K. NDINGO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwanza nitakuomba mwongozo wako kwenye swali hili kwa sababu hizo milioni 360 zilifika katika Shule za Chimala, Igalako, Lujewa na Isitu kujenga madarasa mapya na siyo ukarabati wa shule kongwe. Kwa hiyo baadhi ya madarasa haya 18 yalijengwa kwenye shule hizi. Ninachokitaka mimi kwa Serikali lini wataanza ukarabati wa shule kongwe Mbarali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli, kama ambavyo Mheshimiwa Bahati Ndingo alivyosema kwamba swali lake la msingi ni ukarabati wa shule kongwe, lakini ukarabati unategemea na hali ya uchakavu wa madarasa, yapo madarasa ambayo yamechakaa kiasi cha kutokarabatika beyond repair. Sasa Serikali inachofanya ni kujenga madarasa mengine katika shule hizo na kuvunja madarasa ambayo tayari yamechakaa kiasi hicho.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo hili ndiyo lililofanyika katika shule hizi ikiwa ni sehemu ya ukarabati, lakini hatulazimiki kukarabati madarasa ambayo yana miaka sitini, yameshachokahayakabaratiki tena itakuwa ni matumizi mabaya ya fedha za Serikali. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kukarabati, kama tulivyofanya hivi katika shule hizi kwa namna ya kujenga madarasa mapya au kwa namna ya kukarabati madarasa ambayo yapo katika hali ambayo yanaweza kukarabatika. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, lakini kuna shule ambazo zina hali mbaya sana. Kwa mfano Shule ya Kwemashai, Shule ya Mshizii, Shule ya Msingi Kwai, Shule ya Msingi Matego, Kweboma pamoja na shule nyingine za Jimbo la Lushoto.

Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itapeleka fedha za dharura kwa ajili ya kukarabati shule hizo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; pamoja na uchakavu wa shule lakini unaenda sambamba na ujenzi wa majengo na nyumba za Walimu. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga nyumba za Walimu ili Walimu wetu hawa wasitembee umbali mrefu na vituo vyao vya kazi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ni kweli kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge, amesema kwamba kuna baadhi ya shule ambazo zina uchakavu wa hali ya juu zaidi na kwa kweli zinahitaji bajeti maalum kwa ajili ya kuzikarabati. Kwa hiyo naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inatambua kwamba kuna shule ambazo zinahitaji maalum na tayari imeshaweka mkakati wa ukarabati wa shule hizo.

Mheshimiwa Spika, tumeanza na shule kongwe za sekondari baadhi ya shule zimekarabatiwa, bado nyingi zinahitaji ukarabati, lakini tuna shule nyingi za msingi ambazo tumeanza ukarabati na zoezi hili ni endelevu. Kwa hiyo naomba nitumie nafasi hii kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Lushoto kutuma wahandisi wa halmashauri hiyo ili kufanya tathmini ya mahitaji ya ukarabati kwa shule ambazo Mheshimiwa Mbunge amezitaja na kuwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili fedha iweze kutafutwa, lakini pia kutafutwa mapato ya ndani kwa ajili ya ukarabati.

Mheshimiwa Spika, pili, Serikali imeweka mkakati wa ujenzi wa nyumba za Walimu. Tumeanza kujenga nyumba za three in one, two in one lakini na zoezi hili linaendelea kila bajeti ya kila mwaka, tutahakikisha tunajenga nyumba za Walimu katika shule zetu. Ahsante. (Makofi)
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

Je, ni lini Serikali itakarabati Shule chakavu za Msingi katika Jimbo la Busanda ikiwemo Lubanda, Lulama na nyinginezo nyingi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunatambua katika Jimbo la Busanda pia kuna shule chakavu. Tayari Serikali imeshaanza kuwaainisha shule chakavu zaidi katika majimbo yote kote nchini na fedha zinatafutwa kwa ajili ya kuanza ukarabati kwa awamu. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Jimbo la Busanda pia litapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba kuipongeza Serikali kwa majibu mazuri kuhusiana na miradi hii miwili Mwanhalanga na Ukenyenge.

Mheshimiwa Spika, ninaomba tu kushukuru kwamba shilingi milioni 500 kwa ajili ya Kituo cha Ukenyenge zilijenga yale majengo matano lakini upungufu bado ni mkubwa sana na hivyo kupelekea Kituo hiki kuendelea kubaki na kutokuwa na hadhi kama Kituo cha Afya. Tunahitaji majengo kwa ajili ya wodi za akina mama na akina baba lakini tunahitaji pia walkways kwa baadhi ya Wodi ambazo zitakuwa zinaunganishwa na hizi njia za kuwafikisha Madaktari na wagonjwa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mwanhalanga. Kituo hiki cha afya kina majengo mawili tu na bado wagonjwa ni wengi sana. Ni lini Serikali itakwenda kujenga majengo maalum kwa ajili ya wodi za akina mama, wodi za akina baba, mortuary pamoja na nyumba za watumishi ili tuongeze ari ya watumishi kutenda kazi katika maeneo haya? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Butondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza napokea pongezi zake kwa Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo kwa kweli imefanyika katika Sekta ya Afya kwa ujenzi wa Vituo vya Afya kikiwemo hiki Kituo cha Afya cha Negezi ambacho kimepokea shilingi milioni 500. Ninamhakishia tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunatambua majengo haya bado hayatoshi, hayajakidhi mahitaji, bado tunahitaji wodi, bado tunahitaji mortuary na majengo mengine.

Mheshimiwa Spika, safari ni hatua Mheshimiwa Mbunge, Serikali inaendelea kutenga fedha kwenye bajeti, tuhakikishe kwamba fedha hizi zinapelekwa kwa ajili ya kukamilisha miundombinu hiyo.

Mheshimiwa Spika, pia kuhusiana na Kituo cha Afya cha Mwanhalanga, tunafahamu, tulishapeleka fedha lakini bado kuna majengo ambayo tumeshaweka mpango mkakati kwa ajili ya kutenga fedha ya ukamilishaji. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Mgeta kimejengwa toka mwaka 2018 mpaka leo kimejengwa mortuary imekamilika hakina majokofu manne ya mortuary. Ni lini Serikali itapeleka majokofu manne ya mortuary pamoja na kwamba vituo hivyo vilipewa shilingi milioni 400 ya kujenga na milioni 300 ya vifaa vya tiba...

SPIKA: Umeshauliza swali Mheshimiwa.

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Kituo cha Afya cha Mgeta kimejengwa, kimekamilika, kimeanza kutoa huduma lakini jengo la kuhifadhia maiti limekamilika, tayari Serikali imeshapeleka fedha kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Halmashauri ya Bunda. Moja ya kazi ambayo itafanyika ni kununua jokofu kwa ajili ya kuhifadhia maiti katika kituo hiki cha Mgeta. Ahsante.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Magendo, Kibaha Vijijini tumepokea jokofu la kuhifadhia maiti lakini mortuary haijajengwa; je, lini tutapata pesa kwa ajili ujenzi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwakamo kuwa Serikali ilishatoa maelekezo kwa Halmashauri zetu kote nchini, kwamba Mheshimiwa Rais anapopeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya, lakini anapopeleka fedha kwa ajili ya vifaatiba, kuna baadhi ya miundombinu ambayo iko ndani ya uwezo wa mapato ya ndani ya Halmashauri kama majengo ya mortuary.

Mheshimiwa Spika, natumia fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumuelekeza Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Kibaha, kutenga fedha kwenye mapato ya ndani kujenga jengo la mortuary ambalo ni jengo la gharama ya kawaida kabisa ili wananchi waendelee kupata huduma katika eneo hilo. Ahsante.(Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, Kata ya Susuni na Mwema zilizopo Halmashauri ya Wilaya ya Tarime, hazina kabisa Kituo cha Afya na hivyo kusababisha wananchi kutembea kuja kutafuta huduma Tarime Mjini. Nataka kujua ni lini Serikali itapandisha hadhi Zahanati ya Kiongera ambayo imekarabatiwa ili kuwa Kituo cha Afya na kuweza kurahisisha huduma kwa wananchi hawa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante, ujenzi wa vituo vya afya katika Kata, tunajenga kimkakati, kwanza kwa kufanya tathmini ya vigezo kwa maana ya idadi ya watu, umbali kutoka kituo kingine, pia maeneo yale ambayo ni magumu kufikika. Kwa kuwa, Kata hii ya Susuni na Mwema hatujapata tathmini yake ya kutosha, naomba tuichukue hoja ya Mheshimiwa Mbunge tukafanye tathmini tuone kama inakidhi vigezo, tuziingize kwenye mpango mkakati, aidha kupandisha hadhi zahanati au kufanya ujenzi katika Kata hizo, ahsante.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pamoja na jengo la OPD kukamilika, jengo la wazazi pamoja na upasuaji bado hayajakamilika. Akina mama pamoja na wananchi wanapata adha kubwa kwenda katika hospitali ya wilaya ama kwenda Hospitali ya Rufaa ya Iringa Mjini: Je, lini Serikali itakamilisha majengo haya ili wananchi hao wapate huduma?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, hadi sasa tumebakiza miezi mitano ili tukamilishe mwaka wa fedha na asilimia 100 aliyosema italetwa, bado haijaletwa: Ni lini sasa hiyo fedha asilimia 100 itapelekwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Grace Victor Tendega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimejibu katika majibu yangu ya msingi kwamba ni kweli jengo la OPD limekamilika, jengo la wazazi na upasuaji halijakamilika, na Serikali katika mwaka huu wa fedha imetenga shilingi milioni 100 kwa ajili ya kukamilisha majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia na vile vile nampongeza Mheshimiwa Lukuvi asubuhi ameniambia shilingi milioni 100 tayari imeshapokelewa katika halmashauri yake. Kwa hiyo, nawapongeza kwa ushirikiano huo mzuri wa kuwahudumia wananchi wa Wilaya ya Iringa.

Mheshimiwa Spika, pili, kuhusiana na shilingi milioni 100, ndiyo hiyo ambayo tumeambiwa imeshafika. Kwa hiyo, tutafuatilia utekelezaji ili jengo likamilike mapema wananchi waanze kupata huduma, ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Serikali hii ya Awamu ya Sita inatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Katibu Mkuu Daniel Chongolo ambaye ni mstaafu, alivyopita Jimbo la Kalenga aliahidi kuleta shilingi milioni 500 kujenga Kituo cha Afya Kata ya Lyamgungwe ndani ya miezi mitatu: Je, Serikali itatekeleza lini agizo hili ambalo ni halali kabisa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu inatekeleza kwa ufanisi mkubwa sana Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi na maeneo yote ambayo Serikali imeahidi kujenga vituo vya afya baada ya kujiridhisha na vigezo, tutakwenda kupeleka fedha kwa awamu kwa ajili ya kujenga vituo hivyo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Kiswaga kwamba Ofisi ya Rais, TAMISEMI, itakwenda kufanya tathmini eneo hilo kuona kama linakidhi vigezo na kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya, ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Kata ya Mtwango tumejenga kituo cha afya kwa mapato ya ndani, pia tumejenga jengo kwa ajili ya mortuary, lakini hatuna jokofu. Kwa kuwa nimemsikia Mheshimiwa Waziri kwamba Kibaha Vijijini kuna jokofu na hawana jengo la mortuary; je, Serikali iko tayari kuchukua hili jokofu kwenda pale Mtwango? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza niwapongeze wananchi wa Jimbo la Lupembe na Mheshimiwa Mbunge kwa kujenga Kituo cha Afya cha Mtwango kwa mapato ya ndani. Pia nimhakikishie tu kwamba tunafahamu kwamba kuna jengo la kuhifadhia maiti halina mashine kwa maana ya jokofu la mortuary na tayari Serikali hii imeshapeleka fedha zaidi bilioni 150 kwenye halmashauri zote kote nchini ndani ya miezi mitatu, minne iliyopita kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya kipaumbele yakiwemo majokofu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutatoa kipaumbele kupata jokofu katika Kituo cha Afya cha Mtwango, ahsante. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, swali lilikuwa, kuna jokofu mahali halina chumba, kwa hiyo, limehifadhiwa, halafu kuna mahali kuna chumba ambapo hakuna jokofu. Haliwezi kutolewa hili jokofu ambalo kwa sasa limehifadhiwa halihifadhi maiti likapelekwa kwenye chumba ambacho kipo tayari? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru; jokofu hili lilipelekwa na Bohari ya Dawa kwa maana ya MSD na tulishapata taarifa na tayari taratibu za kulihamisha kupeleka sehemu ambayo tayari jengo limekamilika zinaendelea. Baada ya Kibaha kukamilisha jengo watapelekewa tena jokofu lao. Kwa hiyo, naomba nisilete commitment kwamba tunapeleka Lupembe, lakini tunapeleka sehemu ambayo tayari MSD wameshafanya tathmini na wameona uhitaji kwa sasa ili lisikae bila kufanya kazi, ahsante.
MHE. DANIEL B. SILLO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali ilipeleka shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Gidas: Je, ni lini itamalizia awamu ya pili ya shilingi milioni 250 ili kukamilisha majengo yale?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Sillo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kweli Serikali ilishapeleka shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Gidas na inahitaji shilingi milioni 250 ya awamu ya pili kwa ajili ya ukamilishaji wa majengo yaliyobaki katika hicho kituo cha afya.
Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge wote ambao walipata fedha za awamu ya kwanza ya shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya, kwamba Serikali imeshaweka mkakati katika mwaka ujao wa fedha kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha majengo kwa awamu ya pili. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Makamu wa Rais alipokuja Chiungutwa alitoa ahadi ya shilingi milioni 100 kwa ajili ya kumalizia Kituo cha Afya cha Chiungutwa na pia shilingi milioni 100 pia kwa Kituo cha Afya cha…

SPIKA: Mheshimiwa swali la nyongeza huwa ni moja.

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, lini…

SPIKA: Subiri, subiri. Kwanza huwezi kwenda mbili; pili, kwa sababu ni swali la nyongeza huwezi kuweka maswali mawili katika swali moja. Chagua kimojawapo kati ya hivyo umwulize Mheshimiwa Naibu Waziri ili akujibu.

MHE. ISSA ALLY MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ni lini pesa hizi shilingi milioni 100 zitakwenda kwenye Kituo cha Afya cha Chiungutwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Mchungahela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Mheshimiwa Makamu wa Rais aliahidi shilingi milioni 100 kwa ajili ya ukamilishaji wa Kituo cha Afya cha Chiungutwa na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba fedha hiyo imeshatengwa kwenye bajeti ya mwaka huu 2023/2024 na fedha zitakapopatikana zitapelekwa katika kituo hiki kwa ajili ya ujenzi, ahsante.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Pale kwenye kituo chetu cha Bweri pamoja na Makoko ni vituo ambavyo sasa vimekaa muda mrefu pasipo kumaliziwa; je, ni lini Serikali italeta fedha ili tuweze kumalizia hivyo vituo wananchi waweze kupata huduma bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vedastus Manyinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bweri na Makoko ambavyo havijakamilika, kwanza utaratibu ambao tumeweka Serikalini ni kwamba vituo vyote ambavyo havijakamilika tunafanya tathmini ya kujua havijakamilika kwa sababu gani; je, ni matumizi mabaya ya fedha? Kama ni matumizi mabaya ya fedha tunachukua hatua kwa watumishi waliohusika.

Mheshimiwa Spika, pili, kama ni inatokana na inflation, tumeelekeza halmashauri kutenga fedha kwa awamu, badala ya kusubiri fedha za Serikali kuu pekee kwenda kukamilisha majengo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitumie fursa hii kwanza nichukue hoja hii kwamba tutafanya tathmini kujiridhisha, na pili, nimwelekeze Mkurugenzi wa Halmashauri hii ya Manispaa ya Musoma kuhakikisha wanaanza kutenga fedha kwa ajili ya kukamilisha miundombinu iliyobaki ili vituo vianze kutoa huduma kwa wananchi, ahsante.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa kuwa Serikali ilituahidi kutupatia fedha kwa ajili ya kujenga Kituo chetu cha Afya cha Choma; je, ni lini fedha hizo zitafika kwenye Kituo cha Afya cha Choma? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gulamali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali ilishaahidi kupeleka fedha shilingi milioni 500 kwenye Kituo cha Afya cha Choma na tayari nimeshawasiliana na Mheshimiwa Mbunge mara kadhaa kwamba imeshaingizwa kwenye orodha ya fedha za Benki ya Dunia ambazo tunatarajia wakati wowote mwezi wa Pili au wa Tatu zitatoka kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha afya. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi hiyo imezingatiwa na Serikali itatekeleza, ahsante.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa ujenzi wa soko hili ulitokana na ahadi ya Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan wakati huo akiwa ni Makamu wa Rais; na kwa kuwa Waziri Mkuu alipokuja kwenye ziara wananchi wa Rombo walikumbushia ahadi yao: Je, nini kauli ya Serikali kuhusu ujenzi wa soko hili?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, shilingi milioni 75 ni fedha ndogo sana katika ujenzi huu. Je, Serikali kwa nini isiweke ujenzi wa soko hili katika miradi ya kimkakati ili kutimiza ahadi ya viongozi hawa wawili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie kwamba ahadi za viongozi wetu wa kitaifa ni kipaumbele katika utekelezaji ndani ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa kuwa ni kweli fedha ambayo imetengwa ni kidogo, nitumie fursa hii kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, kumwelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Rombo kufanya tathmini ya kina na upembuzi yakinifu wa gharama zinazohitajika, kwa ajili ya ujenzi wa soko hili na kuziwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili tuweze kuona kama fedha itatoka Central Government au wanaweza kugharamia kwa mapato ya ndani, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa hii nafasi. Halmashauri ya Meru iliwasilisha michoro ya soko la kisasa TAMISEMI mwaka jana mwezi Novemba, kwa maana ya mwaka 2023; soko hili linategemewa kujengwa Eneo la Madira; je, ni lini ujenzi wa soko hili utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante na naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pallangyo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, tulikuwa na utaratibu wa kuwasilisha miradi ya kimkakati lakini tunafanya tathmini na upembuzi kuona kama fedha kwanza ya Serikali ipo, na pia kama halmashauri zenyewe zinaweza zikagharamia kupitia mapato ya ndani. Kwa hiyo, kwa sababu Mheshimiwa Mbunge anatoa taarifa kwamba limeshawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba tulichukue suala, tutalifanyia kazi tufuatilie, andiko liko wapi, limefikia hatua gani, ili tuweze kuona namna gani tunafanya ili kwenda kujenga soka la kisasa katika eneo hili la Madira, ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza kabisa naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kusikia kilio chetu na kuikarabati Hospitali ya Wilaya ya Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa kwa sasa ni ukosefu wa vifaa tiba.

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka vifaa tiba vya kutosha hususan katika Jengo la Mama na Mtoto?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa hospitali hii inakabiliwa na uhaba wa watumishi, ningependa kujua, ni upi mkakati wa Serikali wa kuwapatia watumishi 169 ili kuendana na mahitaji yaliyopo?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aysharose Mattembe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameendelea kujali afya za Watanzania na kupeleka fedha nyingi katika halmashauri zetu kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya huduma za afya. Sambamba na hilo, vifaa tiba vimeendelea kupelekwa katika vituo vilivyokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba Halmashauri ya Manyoni na hospitali hii imeshapokea zaidi ya shilingi milioni 750 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Bado Serikali itaendelea kupeleka fedha kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na vifaa tiba vya kutosha zaidi katika Jengo la Mama na Mtoto na katika majengo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili kuhusiana na upungufu wa watumishi, Serikali imeendelea kuajiri watumishi kwa awamu na kuwapangia katika halmashauri kote nchini ikiwemo Halmashauri hii ya Manyoni. Nimhakikishia kwamba tunatambua kuna upungufu wa watumishi hawa na Serikali itaendelea kuajiri kwa awamu kuhakikisha kwamba watumishi wanapelekwa katika hospitali hii, ahsante. (Makofi)