Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Dr. Festo John Dugange (300 total)

MHE. COSATO D. CHUMI Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza Ujenzi wa Barabara za lami na kufunga taa za barabarani katika Mji wa Mafinga chini ya Mpango wa Uendelezaji Miji nchini?
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu, kwanza naomba nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenijalia mimi na Waheshimiwa Wabunge wote afya njema na kutuwezesha kuwa wawakilishi wa wananchi kupitia Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa imani kubwa aliyonipa kwa kuniteua kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Wanging’ombe kwa kunichagua na kuchagua mafiga matatu ya Chama cha Mapinduzi na niwahakishie utumishi uliotukuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, nijibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi,Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Miji ya Kimkakati (Tanzania Strategic Cities Projects -TSCP) umetekelezwa katika Halmashauri za Majiji ya Tanga, Dodoma, Mbeya, Arusha na Mwanza na Halmashauri za Manispaa za Mtwara- Mikindani, Ilemela na Kigoma-Ujiji kwa gharama ya Dola za Kimarekani milioni 355.5 sawa na shilingi bilioni 799.52.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Kuendeleza Miundombinu katika Miji 18 (Urban Local Government Strengthening Programme - ULGSP) umetekelezwa katika Halmashauri za Manispaa za Morogoro, Tabora, Moshi, Sumbawanga, Shinyanga, Songea, Iringa, Mpanda, Lindi, Singida, Musoma na Bukoba na Halmashauri za Miji Kibaha, Babati, Geita, Korogwe, Bariadi na Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Miji ya Kimkakati (TSCP) pamoja na Mradi wa Kuendeleza Miundombinu katika Miji 18 (ULGSP) ilimalizika muda wake Mwezi Desemba, 2020. Serikali inaendelea na mazungumzo na Benki ya Dunia kwa ajili ya kuanza kutekeleza Programu nyingine ya kuendeleza miundombinu itakayohusisha Halmashauri26 zilizokuwepo kwenye Programu zilizomalizika pamoja na Halmashauri nyingine 19 za Miji ikiwemo Mafinga.
MHE.DKT. PINDI H. CHANA Aliuliza:-

Serikali imekuwa ikisaidia sana vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu nchini kupitia Halmashauri za Wilaya:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha Mifuko hiyo ili kutoa viwango vikubwa zaidi vya mikopo?
NAIBU WAZIRI, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI,naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pindi Hazara Chana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu inayotokana na asilimia 10 ya mapato kutokana na vyanzo vya ndani vya halmashauri inatolewa na halmashauri zote nchini kutokana na fedha zilizokusanywa na halmashauri kwa kipindi husika baada ya kutoa vyanzo lindwa kama vile fedha za uchangiaji wa Huduma za Afya, ada za taka na ada za Shule za Sekondari Kidato cha Tano na Sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha kiwango cha mikopo inayotolewa na halmashauri Serikali imechukua hatua mbalimbali ikiwemo kuzisimamia halmashauri kutekeleza Sheria ya Mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu, kuzijengea uwezo Kamati za Huduma za Mikopo za Kata na Halmashauri ili ziwe na ujuzi wa kutosha wa kuanzisha na kuendeleza vikundi vya wajasiriamali pamoja na ujuzi wa kusimamia utoaji na urejeshwaji wa mikopo, kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wanufaika wa mikopo kabla ya utoaji wa mikopo kupitia Maafisa Maendeleo ya Jamii pamoja na kuzielekeza halmashauri kuendelea kubuni vyanzo vipya vya mapato.
MHE. ANNA R. LUPEMBE Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatengeneza barabara za Kata ya Katumba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS - TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais–TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo ina mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 420.97 ambazo tayari zimeingizwa katika mfumo wa barabara za Wilaya (DROMAS). Aidha, Kata ya Katumba ina mtandao wa barabara zenye urefu wa kilometa 185.88 ambazo ni sawa na asilimia 44 ya mtandao wote.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka wa fedha 2017/ 2018 hadi 2019/2020 Wakala wa Barabara Vijijini na Mijini (TARURA) Wilaya ya Nsimbo umetumia kiasi cha shilingi milioni
246.08 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Msaginya – Kanoge na Ikondamoyo – Kalungu. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 jumla ya shilingi milioni 81.2 imetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Msaginya – Kanoge na barabara ya Kituo cha Afya Katumba – Mto Kalungu.

MheshimiwaSpika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya barabara kote nchini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE (K.n.y. MHE. ALMAS A. MAIGE) Aliuliza: -

Wananchi wa Jimbo la Tabora Kaskazini wamejitolea kujenga Vituo vya Afya katika Kata za llolangulu, Mabama, Shitagena na Usagari katika Kijiji cha Migungumalo: -

Je, Serikali ipo tayari kuanza kuchangia miradi hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athuman Maige, Mbunge wa Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua mchango mkubwa wa wananchi katika ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini. Hivyo, Serikali ina dhamira ya dhati ya kuchangia nguvu hizo za wananchi katika kukamilishaji vituo hivyo ili vianze kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mpango wa ukarabati na ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya nchini ikiwemo kukamilisha maboma ya majengo ya kutolea huduma za afya yaliyojengwa na wananchi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, ambapo ujenzi wake ulisimama kwa kukosa fedha. Hadi kufikia Septemba 2020 jumla ya shilingi bilioni 315.31 zimetumika kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa vituo vya kutolea huduma za afya nchini.

Mheshmiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 27.75 kwa ajili ya kukamilisha maboma 555 ya zahanati nchini yakiwemo maboma manne (04) katika Halmashauri ya Wilaya ya Uyui Mkoani Tabora ili kuunga mkono jitihada za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua na kuthamini michango na nguvu za wananchi na itaendelea kuchangia nguvu za wananchi katika kujenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za afya nchini kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. NAPE M. NNAUYE (K.n.y. MHE. GODWIN E. KUNAMBI) aliuliza: -

Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba ni Halmashauri mpya iliyotoka Wilaya ya Kilombero: -

(a) Je, ni lini Serikali itaipa Mlimba hadhi ya kuwa Wilaya hasa ikizingatiwa umbali mrefu wa takriban Km 200 ambao Wananchi wanatembea kufuata huduma Makao Makuu ya Wilaya?

(b) Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa majengo ya Halmashauri na kuboresha miundombinu ya barabara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godwin Emmanuel Kunambi, Mbunge wa Mlimba lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa miongozo na taratibu, uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala unahusisha uhitaji wa wananchi, Viongozi wa Wilaya na Mkoa ambao huwasilisha maombi ya mapendekezo yao kwenye vikao vya Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) na kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI kwa hatua zaidi. Ofisi ya Rais-TAMISEMI, haijapokea maombi rasmi ya Mkoa wa Morogoro kuomba Mlimba kuwa Wilaya. Serikali inashauri utaratibu huu uliowekwa ufuatwe.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 1.1 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba. Mwezi Januari mwaka huu, Serikali imekwisha peleka kiasi cha shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuanza shughuli za ujenzi wa jengo hilo la utawala.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa miundombinu ya barabara, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020, Serikali imefanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 54, imejenga kalvati 22 na madaraja manne (4) kwa gharama ya shilingi milioni 545.87. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali kupitia TARURA imetenga kiasi cha shilingi milioni 517.56 kwa ajili ya matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba.
MHE. CECILIA D. PARESSO (K.n.y. MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA) Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatengeneza eneo la Katokoro linalounganisha Kata za Katoro na Kyamulaile katika Jimbo la Bukoba Vijijini ili kuondoa adha ya usafiri inayowakabili wananchi wa maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

MheshimiwaSpika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, eneo korofi la Katokoro ambalo limejaa maji lina urefu wa kilomita 5 ambayo ni sehemu ya barabara ya Katoro – Kyamulaile – Kashaba yenye jumla yakilomita 15.7 inayounganisha Kata za Katoro, Kyamulaile na Ruhunga. Aidha, barabara hiyo pia inaunganisha maeneo mbalimbali ya Halmashauriya Wilaya ya Bukoba na Halmashauri ya Wilaya ya Misenyi.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imefanya usanifu kwa ajili ya kuboresha eneo hilo korofi ambapo kiasi cha fedha shilingi milioni 572 kinahitajika kunyanyua tuta la barabara na kujenga makalvati.

Mheshimiwa Spika, ili kupata ufumbuzi kwa sasa katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali ilitenga fedha kiasi cha shilingi milioni 87 kwa ajili ya kurekebisha eneo korofi katika barabara hiyo. Hata hivyo, kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha mkandarasi aliyekuwa anafanya kazi hiyo alisimamishwa kutokana na eneo hilo kujaa maji.

Mheshimiwa Spika, wakati jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya kupata ufumbuzi wa kudumu wa barabara hiyo zikiendelea, mara maji yatakapopungua, mara moja Serikali itamrejesha kazini mkandarasi huyo ili kurejesha mawasiliano katika eneo hilo.
MHE. BENAYA L. KAPINGA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha kuanzia Novemba, 2015 hadi Septemba, 2020, Serikali imejenga Hospitali 101 za Halmashauri na kuongeza idadi ya Hospitali za Halmashauri kutoka Hospitali 77 zilizokuwepo mwaka 2015 hadi Hospitali 178 Septemba, 2020.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya kigezo muhimu kwa Halmashauri kupata fedha za ujenzi ilikuwa ni kuandaa eneo la ujenzi. Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga ilikosa fedha za ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri kwa kuwa hadi wakati wa tathimini ya Halmashauri zilizotenga maeneo ya ujenzi, Hospitali ya Halmashauri ya Mbinga ilikuwa haijapata eneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 27 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali za Halmashauri 27 mpya nchini. Aidha, kwa kuwa sasa tayari Halmshauri ya Wilaya ya Mbinga imebainisha eneo la ujenzi, Serikali itaipa kipaumbele sambamba na Halmashauri nyingine ambazo hazina Hospitali za Halmashauri kwenye awamu zinazofuata kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA Aliuliza:-

Je ni lini Serikali itajenga chumba cha kuhifadhia maiti kwenye Hospitali ya Wilaya ya Mbogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Mbogwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2019/2020, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hospitali ya halmashauri. Majengo yaliyohusika katika awamu ya kwanza ni jengo la wagonjwa wa nje na maabara. Ujenzi wa majengo hayo upo katika hatua ya ukamilishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 60.5 ambapo kiasi cha shilingi 33.5 ni kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa hospitali za halmashauri 67 nchini na kiasi cha shilingi bilioni 27 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa hospitali za halmashauri 27 mpya ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe iliyotengewa kiasi cha shilingi bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe inaelekezwa pamoja na majengo mengine, kujenga jengo la kuhifadhia maiti pindi itakapopokea fedha za ujenzi kwa kuwa tayari ina majengo mawili kati ya majengo saba yanayotakiwa kujengwa na hivyo fedha iliyotengwa kwenye bajeti ya mwaka 2020/2021 itakuwa sehemu ya fedha ya kujenga jengo la kuhifadhia maiti.
MHE. JAFARI W. CHEGE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Daraja la Mto Mori kwani mto huo umekuwa ukisomba watu na kusababisha vifo kwa wananchi wanaofuata huduma upande wa pili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Mori unakatisha katika barabara ya Kirogo-Nyamaguku yenye urefu wa kilomita 15, ikiunganisha Tarafa za Luo-imbo, Suba na Nyancha katika Wilaya ya Rorya. Barabara hii ilifunguliwa mwaka 2008 kwa nguvu za wananchi kupitia Mpango wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto huu umegawanyika katika matawi mawili ambayo ni Mto Mori Mkuu wenye upana wa mita 43 na Wamala wenye upana wa mita 16 ambapo madaraja mawili (2) yanahitajika kujengwa. Hivyo, kwa sasa, barabara hii haipitiki kutokana na kutokuwepo kwa madaraja hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na umuhimu wa barabara hiyo, Halmashauri ya Wilaya ya Rorya imewasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI, maombi maalum ya Shilingi bilioni 1.54 ambayo ni makisio kwa ajili ya ujenzi wa daraja katika Mto Mori na matengenezo ya kawaida katika Barabara ya Nyamaguku- Kirogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itatenga fedha kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kwa ajili ya usanifu wa madaraja mawili ya Mto Mori ili kufahamu mahitaji na gharama halisi za ujenzi wa madaraja hayo na kisha kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi. Aidha, ujenzi wa madaraja na miundombinu ya barabara hizi utatekelezwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ASIA A. HALAMGA Aliuliza:-

Ni Halmashauri ngapi nchi zimetekeleza kwa asilimia 100 sheria ya utoaji mikopo asilimia 10 ya makusanyo ya ndani kwa makundi ya vijana, akinamama na watu wenye mahitaji maalum?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asia Abdukarim Halamga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimwa Naibu Spika, kwa mujibu wa takwimu zilizopo hali ya utoaji wa mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu katika Halmashauri nchini imeimarika hasa baada ya kufanya marekebisho ya Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura 290 yaliyofanyika Julai, 2018 kwa kuongeza Kifungu cha 37A kuhusu Mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu.

Mheshimwa Naibu Spika, tangu kuanza kutumika kwa Sheria hii mwaka wa fedha 2018/2019 na 2019/2020 Halmashauri 79 zimetoa mikopo kwa asilimia 100 na Halmashauri 54 zimetekeleza kwa asilimia zaidi ya 85.

Mheshimwa Naibu Spika, utekelezaji wa shughuli hizi za mikopo umewezesha kuongezeka kwa mikopo inayotolewa na halmashauri nchini ikilinganishwa na kipindi kabla ya kufanya marekebisho ya sheria. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 (kabla ya marekebisho ya sheria) shilingi bilioni 26.1 zilitolewa; mwaka wa fedha 2018/2019 (baada ya marekebisho ya sheria) shilingi bilioni 42.06 zilitolewa; na mwaka wa fedha 2019/2020 jumla ya mikopo iliyotolewa ilikuwa ni shilingi bilioni 40.7 zilitolewa.

Mheshimwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Kifungu namba cha 24(2) cha Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu za mwaka 2019, Mkurugenzi yeyote ambaye atashindwa kusimamia utekelezaji wa Kanuni hizi atakuwa ametenda kosa la kinidhamu na mamlaka yake ya nidhamu inaweza, kwa kadri itakavyoona inafaa, kumchukulia hatua za kinidhamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo naomba kutoa rai kwa Wakurugenzi wote nchini kote kuhakikisha kwamba wanazingatia takwa hilo la kisheria.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE (K.n.y. MHE. SILVESTRY F. KOKA) Aliuliza:-

Miundombinu ya maji katika Shirika la Elimu Kibaha ilijengwa miaka 50 iliyopita kwa kutumia mabomba ya Asbestos ambayo siyo rafiki kwa afya za binadamu, lakini pia ni chakavu sana:-

(a) Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika shirika hilo?

(b) Je, ni lini Serikali itakarabati majengo ya Chuo cha FDC katika Shirika hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya maji katika Shirika la Elimu Kibaha inayotokana na miundombinu mibovu na ya muda mrefu ambayo ni kutokana na uwepo wa mabomba ya maji ya kipenyo cha milimita 200 yenye urefu wa kilomita nne na kipenyo cha milimita 150 yenye urefu wa kilomita mbili yaliyojengwa kwa asbestos tangu kuanzishwa kwa Shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali ilikwishabadilisha bomba la asbestos lenye urefu wa kilomita 0.75 la kipenyo cha milimita 200 na bomba lenye urefu wa kilomita moja na kipenyo cha milimita 150 kuwa PVC. Serikali itaendelea kubadilisha mabomba hayo kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Shirika linaendelea kufanya matengenezo madogo madogo kwa kutumia mapato ya ndani pindi uharibifu unapotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa shirika hili, imekamilisha ukarabati wa Shule ya Sekondari Kibaha kwa gharama ya Shilingi bilioni 1.6. Vilevile katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 80 kwa ajili ya ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya tathmini ya ukarabati wa miundombinu ya majengo ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Shirika la Elimu Kibaha ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.48 kinahitajika ili kufanya matengenezo. Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati. Hata hivyo, Shirika la Elimu Kibaha lilifanya ukarabati mdogo wa madarasa na jengo la utawala kwa kutumia mapato ya ndani ambao uligharimu shilingi milioni 25.73.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID Aliuliza:-

Je, ni lini utekelezaji wa ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne ya kujenga Daraja la Mto Pangani mpakani mwa Wilaya za Same na Simanjiro utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais –TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mto Pangani umekatisha kwenye kipande cha barabara ya Same – Ruvu – Mferejini chenye urefu wa kilomita 34.2. Barabara hiyo inaunganisha Kata za Same na Ruvu katika Wilaya ya Same na sehemu ya mto inayopendekezwa kujengwa daraja ina upana wa mita 70. Sehemu hii haipitiki kwa sasa kutokana na kukosekana kwa daraja la kuunganisha Wilaya ya Same, Mkoa wa Kilimanjaro na Wilaya ya Simanjiro Mkoa wa Manyara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) imekuwa ikikihudumia kipande cha barabara hiyo kwa kufanya matengenezo kwenye maeneo korofi ambapo katika mwaka wa fedha 2018/2019 kiasi cha shilingi milioni 48 kilitumika. Aidha, katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021 kiasi cha shilingi milioni 63 kimetengwa kwa ajili ya matengenezo ambapo kwa sasa mkandarasi anaendelea na matengenezo ya kipande cha kilomita 7.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/22, Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) umepanga kufanya usanifu wa daraja ikiwa ni pamoja na kipande cha barabara yenye urefu wa kilomita 34.2 kwa upande wa Same hadi kufikia eneo la Mto Pangani panapohitajika kujengwa daraja ili kuunganisha Wilaya za Same na Simanjiro. Serikali itatoa kipaumbele cha ujenzi wa daraja na miundombinu ya barabara hiyo muhimu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA Aliuliza:-

Halmashauri ya Wilaya ya Newala ina Kata 22 na Vijiji 107, lakini ina Vituo vya Afya vitatu tu, kati ya 22 vinavyohitajika.

Je, Serikali haioni haja ya kujenga Vituo vipya vya Afya katika Halmashauri ya Newala ili kuboresha huduma za Afya kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maimuna Salum Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza Mpango wa Maendeleo wa Afya ya Msingi (MMAM) kwa kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Kuanzia mwaka 2015 hadi Septemba 2020, Serikali imejenga Zahanati 1,198; imejenga na kukarabati Vituo vya Afya 487 na imejenga Hospitali za Halmashauri102.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 na 2019/2020, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Newala kiasi cha Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri na Shilingi milioni 400 kwa ajili kufanya ukarabati wa Kituo cha Afya Kitangari. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha Shilingi bilioni moja (1) kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri na Shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya Zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Newala.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya nchini kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. GRACE V. TENDEGA Aliuliza:-

Akina mama wajawazito wamekuwa wakitozwa fedha kuanzia shilingi 50,000/= hadi 70,000/= wasipojifungulia katika Vituo vya Afya hasa katika Jimbo la Kalenga; huku vituo hivyo vikiwa mbali na maeneo wanayoishi.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga maeneo ya kusubiri kujifungua katika Vituo vya Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, majengo ya wajawazito kujisubiria yanalenga kupunguza umbali kwa wajawazito kufika kwenye vituo vya huduma za afya pindi wanapokaribia kujifungua. Lengo likiwa ni kupunguza vifo vya akina mama wajawazito na watoto wachanga vinavyosababishwa na umbali kutoka katika vituo vya kutolea huduma.

Meshimiwa Spika, katika kutatua changamoto hii, Serikali imeendelea kujenga vituo vya huduma za afya kote nchini na kujenga Hospitali za Halmashauri 102, Vituo vya Afya 487 na Zahanati 1,198 katika kipindi cha Novemba, 2015 hadi Septemba, 2020. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali za Halmashauri 67; shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali 67 za Halmashauri na shilingi bilioni 27 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali mpya za Halmashauri. Kiasi cha shilingi bilioni 27.5 pia kimetengwa kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati 555.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mpango wa ujenzi na ukarabati wa Vituo vya Afya nchini kote, umepunguza umbali kwa wananchi kuvifikia vituo vya huduma za afya na hivyo viashiria vya huduma na vifo vya wajawazito vimepungua kutoka 11,000 mwaka 2015 hadi 3,000 mwaka 2020. Serikali itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya huduma za afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. ESTHER L. MIDIMU K.n.y. MHE. SIMON S. LUSENGEKILE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa katika Hospitali ya Wilaya ya Busega ili huduma bora za afya ziendelee kutolewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Busega ni miongoni mwa hospitali 67 za Halmashauri zilizoanza kujengwa mwaka 2018/2019 kwa kupewa fedha kiasi cha shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa majengo saba ambayo ni jengo la utawala, jengo la wagonjwa wa nje, jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la wazazi, jengo la kufulia na jengo la kuhifadhia dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali 67 za Halmashauri ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Busega ambayo imetengewa shilingi milioni 500.

Vilevile katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika hospitali 67 za Halmashauri ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Busega ambayo imetengewa shilingi milioni 500.
MHE. ZAYTUN S. SWAI Aliuliza:-

Kutokana na changamoto za vyanzo vya mapato hususan katika Halmashauri zilizo nje ya miji kumekuwa na uwiano usio sawa wa utoaji wa mikopo.

Je, Serikali haioni umuhimu wa kutafuta njia ya kuweka uwiano sawa wa mikopo hiyo bila kujali mapato ya Halmashauri husika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mikopo ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri hutolewa kwa kuzingatia kifungu cha 37A cha Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura 290 na Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu za mwaka 2019. Halmashauri inatakiwa kutenga na kutoa asilimia 10 ya fedha za makusanyo ya ndani katika kipindi husika kwa ajili ya mikopo ya vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu baada ya kuondoa vyanzo lindwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, msingi wa sheria hii ni asilimia 10 ya mapato yanayokusanywa kwenye Halmashauri husika ambayo yanatofautiana kati ya halmashauri moja na nyingine kutokana na fursa zilizopo. Hivyo, kiwango cha mikopo inayotolewa kinategemea uwezo wa makusanyo wa Halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa utoaji wa mikopo kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu umeendelea kuimarika mwaka hadi mwaka hususan baada ya kuwepo kwa sheria ambapo mikopo imeongezeka kutoka shilingi bilioni 26.1 mwaka 2017/2018 hadi shilingi bilioni 42.06 mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio hayo Serikali inatambua changamoto zinazotokana na utaratibu huu na itaendelea kuuboresha ili kuongeza tija na kufikia malengo ya kuwawezesha wananchi kiuchumi kupitia mikopo hii.
MHE. FLATEI G. MASSAY (K.n.y. MHE. ZACHARIA P. ISSAAY) Aliuliza:-

Mwaka 2015 Serikali ilitangaza kugawa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na kupitia vikao vya Mabaraza ya Madiwani wa Halmashauri za Mbulu Wilaya na Mbulu Mji walipitisha rasmi mgawanyo wa rasilimali na madeni.

Je, ni lini Serikali itarejesha tamko la mapendekezo hayo ili kufanikisha maendeleo ya mambo yaliyopendekezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay, Mbunge wa Mbulu Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu kupitia vikao vya Mabaraza ya Madiwani wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu na Halmashauri ya Mji Mbulu waliridhia na kupitisha mgawanyo wa rasilimali na madeni na kuwasilisha mgawanyo huo Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Tarehe 9 Novemba, 2018 mgawanyo wa mali na madeni ya Halmashauri hizo ulitolewa na Waziri mwenye dhamana na kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali Toleo Namba 45 la mwaka 2018 pamoja na mgawanyo wa mali na madeni wa Halmashauri nyingine 42 kupitia Tangazo la Serikali Namba 696 la mwaka 2018.

Mheshimiwa Naibu Spika, mgawanyo wa rasilimali watu, magari, pikipiki, rasilimali na madeni umefanyika kwa asilimia 100 kwa kuzingatia Mwongozo wa Ugawaji wa Mali na Madeni ulioandaliwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI wa mwaka 2014. Katika mgawanyo huo, Halmashauri ya Wilaya ya Mbulu (Halmashauri mama) ilipata asilimia 60 na Halmashauri ya Mji wa Mbulu ilipata asilimia 40.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa fedha ili kukamilisha ujenzi wa Ofisi ya Halmashauri ya Wilaya ya Magu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniventura Destery Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka mitano iliyopita Serikali imeendelea na ujenzi wa majengo ya utawala katika Halmashauri 100 ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Magu ambazo kwa ujumla zimegharimu kiasi cha shilingi bilioni 147.33.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Magu ambalo litagharimu shilingi bilioni tano hadi kukamilika. Hadi mwezi Februari 2021, Serikali ilikuwa imekwishatoa shilingi bilioni tatu kwa ajili ya ujenzi wa jengo hilo ambalo tayari limeezekwa. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 750 kwa ajili ya kuendelea na hatua ya ukamilishaji wa jengo hilo.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Hospitali ya kisasa Mkoani Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na mpango wa kujenga Hospitali za kisasa za Halmashauri na za Rufaa za Mikoa ili kuboresha huduma za afya za rufaa katika ngazi hizo. Kupitia mpango huo, Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro itakarabatiwa na kupanuliwa. Mpango huo utahusika ujenzi wa jengo la kisasa la wagonjwa wa nje, jengo la kutolea huduma za dharura, jengo la huduma za uchunguzi wa mionzi na maabara, matibabu ya viungo, huduma za famasia, utawala pamoja na Wodi Maalum (Private Wards).

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa eneo ilipo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kwa sasa ni dogo, Serikali kupitia Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Morogoro inakamilisha taratibu za umiliki wa eneo lenye ukubwa wa ekari 100 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa ya kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile katika kuboresha huduma za afya ngazi ya msingi katika Mkoa wa Morogoro, Serikali imejenga Hospitali tano za Halmashauri ya Malinyi, Gairo, Morogoro, Mvomero na Kilombero kwa gharama ya shilingi bilioni 7.5 katika kipindi cha Juni, 2016 hadi Juni, 2020. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni mbili kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali za Halmashauri ya Mlimba na Mvomero. Aidha, shilingi bilioni 1.5 zimetengwa kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa wodi tatu katika Halmashauri za Wilaya za Malinyi, Gairo na Morogoro.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaboresha Hospitali ya Wilaya ya Olturumet katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha kwa kuipatia jengo la OPD, Wodi ya kulaza Wagonjwa, Jengo la X-Ray na mashine ya X-Ray ili Hospitali hiyo iweze kutoa huduma kwa wananchi ipasavyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemberis Saputu Mollel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uwepo wa Hospitali kongwe 43 za Halmashauri nchini ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Olturumet Arusha, ambazo zinahitaji ukarabati na upanuzi wa miundombinu ili kuendana na mahitaji ya sasa ya utoaji wa huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza Mpango wa Ukarabati wa Hospitali kongwe 43 nchini ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itaomba kutengewa kiasi cha shilingi bilioni 11 kwa ajili ya kuanza ukarabati wa Hospitali 21 za Halmashauri nchini. Mpango huo utaendelea kutekelezwa kwa awamu hadi ukarabati na upanuzi wa hospitali kongwe zote nchini utakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge Noah kuwa Hospitali ya Wilaya ya Olturumet Arusha ni miongoni mwa hospitali ambazo zitafanyiwa ukarabati na upanuzi.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA Aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi na vifaa muhimu kwenye hospitali inayojengwa katika Mji wa Tunduma ili ianze kufanya kazi mapema?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza madaktari na wakunga pamoja na kuongeza bajeti katika Kituo cha Afya cha Tunduma ili kukidhi mahitaji ya kituo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa tangu Mheshimiwa Rais aliponipa dhamana ya kumsaidia kama Naibu Waziri, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini nimuahidi kwamba nitafanya kazi kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Tunduma ambayo ilianza kujengwa katika mwaka wa fedha 2016/2017. Ujenzi wa awamu ya kwanza unahusisha jengo la ghorofa moja lenye sehemu tisa za huduma mbalimbali za OPD ambalo limetumia shilingi bilioni nne ambalo hadi Machi, 2021 ujenzi wake umefikia asilimia 82.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itaomba kuidhinishiwa shilingi bilioni moja kwa ajili ya kukamilisha ujenzi na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Baada ya kukamilisha ujenzi huo Serikali itapeleka watumishi na huduma za OPD zitaanza kutolewa. Serikali imeshawapanga madaktari wawili katika hospitali hii ambao kwa sasa wanaendelea kutoa huduma kwenye Kituo cha Afya Tunduma wakisubiri kukamilika kwa Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Tunduma kina jumla ya watumishi 74 kati ya watumishi 52 wanaohitajika katika ngazi ya kituo cha afya na hivyo kuwa na ziada ya watumishi 22. Idadi ya watumishi waliozidi inatokana na kituo hiki kutumika kama Hospitali ya Mji wa Tunduma. Hivyo, watumishi hawa watahamishiwa katika hospitali mpya ya mji mara itakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali itaomba kuindhinishiwa shilingi milioni 409 kwa ajili ya dawa na vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Tunduma ambalo ni ongezeko la shilingi milioni 84 ikilinganishwa na bajeti ya shilingi milioni 325 iliyoidhinishwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa mradi wa kimkakakti wa machinjio Iringa Ngelewala ili kuwekezaji huo uanze kuleta tija kwa Taifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathan Msambatavangu, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Iringa ilianza ujenzi wa machinjio ya Ngelewala katika mwaka wa fedha 2008/2009. Hadi Juni, 2018 kiasi cha shilingi milioni 928.99 kilikuwa kimetumika ikiwemo shilingi milioni 550 kutoka Serikali Kuu, shilingi milioni 108 mapato ya ndani ya Halmashauri, shilingi milioni 101 kupitia programu ya kuendeleza kilimo nchini ASDP na shilingi milioni 169 kutoka UNIDO.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 mradi huu ulijumuishwa kwenye miradi ya kimkakati ya Halmashauri inayotekelezwa ili kuziongezea Halmashauri uwezo wa kutoa huduma na kukusanya mapato. Miundombinu ambayo tayari imejengwa ni pamoja na mabwawa ya maji machafu (oxidation ponds), zizi la kuhifadhia mifugo kabla ya kuchinjwa, shimo la kutupa nyama isiyofaa kuliwa na binadamu, jengo la utawala, uzio eneo la shughuli za dobi, kichomea taka, maabara na jengo la kubadilishia mavazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi mradi kukamilika kwa kujenga miundombinu yote, utagharimu shilingi bilioni 1.147. Mkandarasi anaendelea na ujenzi na anatarajiwa kukamilisha mradi ifikapo tarehe 1 Agosti, 2021.
MHE. KENNETH E. NOLLO Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanzisha mfumo wa ukusanyaji mapato wa GoTHOMIS kwenye zahanati kama ilivyo kwenye vituo vya afya ili kuondoa mwanya wa upotevu wa mapato?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kenneth Ernest Nollo, Mbunge wa Jimbo la Bahi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mfumo wa Kieletroniki wa Uendeshaji wa Huduma za Afya (Government of Tanzania Health Operations Management Information System - (GoTHOMIS) ni mfumo wa usimamizi wa uendeshaji wa vituo vya kutolea huduma za afya, ikiwa ni pamoja na kukusanya taarifa za wagonjwa na magonjwa, taarifa za malipo ya matibabu, taarifa za madawa na vifaa tiba na taarifa za huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfumo huu ulianzishwa mwaka 2016 na kuanza kusimikwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika ngazi zote. Mfumo umeboreshwa na kuunganishwa na mifumo mingine kama Mfumo wa Malipo ya Serikali (GePG), mfumo wa NHIF kwa ajili ya usimamizi wa madai na mfumo wa Kuomba Madawa kutoka Bohari Kuu ya Dawa (ELMIS).

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi Februari 2021, Mfumo wa GoTHOMIS umesimikwa katika vituo vya kutolea huduma 921, ikiwa ni hospitali 21 za mikoa, hospitali 82 za halmashauri, hospitali teule za wilaya 22, vituo vya afya 385 na zahanati 411. Kazi ya kusimika mfumo huu katika vituo vya kutolea huduma za afya katika ngazi zote nchini inaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri zimekuwa zikitumia vyanzo vyake vya ndani kusimika mtandao kiwambo na kununua vifaa vingine zikiwemo kompyuta na wataalam wa halmashauri kushirikiana na wataalam wa mikoa katika kusimika mifumo hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya vituo vilivyofungiwa Mfumo wa GoTHOMIS na ambavyo vina miundombinu wezeshi kama mawasiliano ya internet vinatumia moja kwa moja Mfumo wa Kielektroniki wa Ukusanyaji wa Mapato ya Serikali (GePG) na hivyo kuwezesha wapewa huduma kulipa moja kwa moja benki au kupitia mitandao ya simu na hivyo kuwezesha makusanyo ya vituo kuongezeka na kutumika ipasavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ufungaji wa mifumo huu utaendelea kutekelezwa.
MHE. CECILIA D. PARESSO K.n.y. MHE. ALLY J. MAKOA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakarabati au kujenga Hospitali mpya ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa kwa kuwa Hospitali iliyopo ni ya muda mrefu na miundombinu yake ni chakavu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Kondoa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa hospitali kongwe na chakavu katika baadhi ya Halmashauri nchini ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali za Halmashauri 102 ambazo zipo katika hatua mbalimbali za ujenzi. Kwa kuwa, bado kuna Halmashauri 28 zisizo na Hospitali ya Halmashauri, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga kiasi cha shilingi bilioni 14 ili kuanza ujenzi katika Halmashauri hizo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka kipaumbele kwa kuanza ujenzi katika Halmashauri hizo na baada ya hapo ukarabati wa Hospitali chakavu ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa utafanyika. Ahsante sana.
MHE. BAHATI K. NDINGO Aliuliza: -
Je, ni lini Serikali itakamilisha uanzishwaji wa hati fungani za Serikali za Mitaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, wakati wa kuwasilisha hotuba ya bajeti ya Serikali ya mwaka wa fedha 2021/22 Waziri wa Fedha na Mipango aliwasilisha kuhusu kuanzisha hati fungani za Halmashauri. Kifungu cha 92 ya hotuba yake ilieleza, katika jitihada za kupanua wigo wa vyanzo vya mapato rasilimali fedha Serikali itaangalia uwezekano wa kutumia hati fungani zitakazotolewa na Halmashauri za Manispaa na Majiji kama njia mbadala ya kupata rasilimali fedha kwa ajili ya miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Spika, hatua hii itapunguza mzigo kwenye mfuko mkuu wa Hazina ya Serikali hasa kwa Halmashauri zenye miradi ambayo imefanyiwa upembuzi yakinifu na kuwa na uhakika wa uwezo wa miradi hii kurejesha kwa faida kwa maana ya bankable projects.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Mfuko wa Maendeleo wa Umoja wa Mataifa (United Nations Capital Development Fund – UNCDF) na Mamlaka ya Usimamizi wa Masoko ya Mitaji (Capital Markets and Securities Authority- CMSA) imeanza mchakato wa kupitia miradi ya Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuhakikisha Halmashauri za Miji, Manispaa na Majiji yatakayokidhi vigezo na masharti ya matumizi ya hati fungani yanaanza kutumia utaratibu huu katika mwaka huu wa fedha 2021/2022. Ahsante sana.
MHE. ANTON A. MWANTONA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapima maeneo yote ya umma ikiwemo Shule, Vituo vya Afya na Zahanati kwa kutumia Sheria Na. 4 na Na. 5 ili kuondokana na matatizo ya migogoro ya mipaka kwa Wananchi, lakini pia kuondokana na hoja za ukaguzi ambazo zaidi ya asilimia 90 ya Halmashauri wanazipata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, ninaomba kujibu Swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa baadhi ya maeneo ya umma yaliyoainishwa na kutengwa kwa ajili ya utoaji wa huduma mbalimbali za umma zinazotolewa na Serikali Kuu na Mamlaka za Serikali za Mitaa hayajapimwa na kuwekewa alama zinazoonekana kwa urahisi. Hali hii husababisha migogoro ya mara kwa mara ya ardhi na uvamizi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hizo Serikali imezielekeza halmashauri zote nchini kutenga fedha kila mwaka katika bajeti zao kwa ajili ya kupima maeneo yote ya taasisi za umma zilizo chini ya mamlaka hizo; ikiwa ni pamoja na kuweka alama zinazoonekana kwa urahisi ili kuepusha migogoro ya ardhi na kuzuia uvamizi unaofanywa na baadhi ya wananchi. Serikali ilishatoa maelekezo haya kwa Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa; hivyo nitumie fursa hii kuzisisitiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha zinatenga fedha na kutekeleza maelekezo hayo. Ahsante sana.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani kutatua migogoro ya ardhi kati ya wawekezaji katika kilimo na wananchi wa Kata za Kapele, Ndalamo, Ikama, Nzoka, Msanyani na Kamsamba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe, Mbunge wa Momba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Wilaya ya Momba kumekuwa na migogoro ya ardhi kati ya wawekezaji katika kilimo na wananchi katika Kata za Kapele, Ndalamo, Ikama, Nzoka, Msanyani na Kamsamba. Migogoro hii imetokana na uuzaji holela wa ardhi uliokuwa unafanywa na baadhi ya viongozi wa vijiji katika kata hizo.

Mheshimiwa Spika, ili kutatua migogoro hiyo, Serikali kupitia Sekretarieti ya Mkoa wa Songwe pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Momba imefanya uhakiki na kubaini jumla ya migogoro 38. Kati ya migogoro hiyo, migogoro 34 tayari imetatuliwa na migogoro minne ipo katika hatua mbalimbali za utatuzi.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu rasmi wa kisheria katika uuzaji na ukodishaji ardhi ili kuepusha migogoro kati ya wawekezaji na wananchi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU Aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka Watumishi na Vitendea kazi vya kutosha katika Zahanati mpya 24 zilizojengwa ndani ya Halmashauri ya Mji wa Geita?

(b) Je, ni lini Serikali itadhibiti upotevu wa mapato katika Zahanati, Vituo vya Afya hadi Hospitali za Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu Mbunge wa Geita Mjini lenye sehemu (a) and (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Geita ina jumla ya watumishi 162 wa kada mbalimbali ya afya na upungufu wa watumishi 469. Mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali iliajiri watumishi 2,726 na kupanga katika vituo vilivyokuwa na upungufu mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 halmashauri imeomba jumla ya watumishi 126. Aidha, Serikali inaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa afya katika kuendelea kupunguza changamoto ya upungufu wa watumishi, ikiwemo watumishi kwenye Halmashauri ya Mji Geita.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kudhibiti upotevu wa mapato kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini ambapo hadi Februari 2021, mfumo wa GoTHOMIS umesimikwa katika hospitali 21 za Mikoa, Hospitali 82 za halmashauri, hospitali teule za Wilaya 22, Vituo vya Afya 385 na zahanati 411. Aidha hatua za kinidhamu na kisheria zinaendelea kuchukuliwa kwa watumishi wanaothibitika kuhusika na upotevu wa mapato.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji Geita inaendelea kufunga mfumo wa ukusanyaji wa taarifa za Afya na fedha ili kuboresha ukusanyaji wa mapato katika vituo vya kutolea huduma za afya, ambapo kwa mwaka wa fedha 2021/2022 shilingi milioni 28.2 zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa Mfumo wa ukusanyaji wa mapato (GoTHoMIS) katika Zahanati 11 kati ya Zahanati 13 zilizopo ambazo hazina Mfumo wa GOT- HOMIS. Hospitali ya Geita pamoja na Vituo viwili vya Afya vilivyopo tayari vimefungwa mfumo wa GoTHOMIS. Ahsante sana.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Hayati Dkt. John Magufuli, Makamu wa Rais wa sasa na Waziri Mkuu ya kujenga Kituo cha Afya Kata ya Murungu katika Wilaya ya Kibondo ili kusogeza huduma na kupunguza msongamano wa wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Kibondo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga na kukarabati Vituo vya Kutolea huduma za Afya kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuboresha utoaji wa Huduma za Afya ya Msingi kwa wananchi ikiwemo upatikanaji wa huduma za upasuaji. Ujenzi na ukarabati wa huo unahusisha pia utekelezaji wa ahadi za Viongozi Wakuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, Katika kutekeleza mkakati huu, Serikali imepeleka fedha shilingi bilioni 25.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Vituo vya Afya kwenye Tarafa 90 zisizo na Vituo vya Afya ikiwemo Tarafa ya Kibondo Mjini inayoundwa na Kata tisa za Murungu, Bunyambo, Kibondo Mjini, Biturana, Kumwambu, Kitahana, Rusohoko, Misezero na Bitare ambapo kiasi cha shilingi milioni 250 kimepelekwa kwa jili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Bunyambo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na utekelezaji wa mkakati huu, Serikali, itaendelea kutoa fedha kwenye halmashauri kwa ajili ya utekelezaji wa ahadi zote za Viongozi.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia ujenzi wa Jengo la Manispaa ya Tabora ambao umesimama kwa muda mrefu sasa huku shughuli za Manispaa zikiendelea kufanyika kwenye majengo ya zamani yaliyochakaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mhesimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa baadhi ya halmashauri nchini ambazo hazina majengo ya utawala na uwepo wa majengo chakavu. Serikali kwa kutambua hilo, inaendelea na ujenzi wa majengo ya utawala ya Halmashauri 100 nchini kote ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Tabora.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa Tabora kwa kutumia mapato ya ndani, mwaka 2015 ilianza kujenga jengo la utawala la ghorofa nne ambalo lilikadiriwa kugharimu kiasi cha shilling bilioni 5.7 mpaka litakapokamilika. Ujenzi wa awamu ya kwanza unaohusisha boma la jengo hilo umekamilika.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo, katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga kiasi cha shilingi bilioni moja ili kuendeleza ujenzi wa jengo hilo ambapo ujenzi wa awamu ya pili utatumia utaratibu wa force account ili kupunguza gharama za ujenzi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Tabora, imeelekezwa kukamilisha taratibu za kuwasilisha maombi ya fedha za ujenzi huo Wizara ya fedha na Mipango ili ujenzi uanze mara moja.

Mheshimiwa Spika, aidha, halmasahuri imeelekezwa kuanza ukamilishaji wa baadhi ya maeneo ya jengo hilo ili watumishi waweze kupata ofisi wakati ukamilishaji ukiendelea.
MHE. FATMA H. TOUFIQ K.n.y. MHE. MOHAMED L. MONNI Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kujenga stendi katika Mji wa Chemba ambao unakuwa kwa kasi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu wa Wilaya ya Chemba kuwa na kituo cha kisasa cha mabasi. Kwa umuhimu huo Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Chemba imetenga eneo la ekari 22 kwa ajili ya ujenzi wa stendi kuu ya mabasi katika Mji wa Chemba ambayo imekadiriwa kugharimu kiasi cha shilingi milioni 643.8 mpaka kukamilika kwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Halmashauri ilitenga kiasi cha shilingi milioni 37 kutoka katika mapato yake ya ndani kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi hiyo ambapo ujenzi wa vyoo na ofisi za muda umekamilika kwa gharama ya shilingi milioni saba ili kuwezesha wananchi kuanza kupata huduma za stendi. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni 16 ili kuendeleza ujenzi wa stendi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa utekelezaji wa miradi ya kimkakati unahusisha andiko maalum la mradi linaloandaliwa na Halmashauri na kuwasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Chemba kufuata utaratibu huo ili Serikali itafute fedha kwa ajili ya kutekeleza mradi huo. Ahsante sana.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. MICHAEL M. KEMBAKI Aliuliza: -

Serikali ilichukua eneo la Mlima Nkongore ambao ndani yake kulikuwa na makazi ya wananchi na kuliwekea beacon na kusababisha kaya zaidi ya 10 zilizochukuliwa maeneo hayo kuishi kwa hofu.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzilipa fidia Kaya hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Mwita Kembaki, Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mlima Nkongore uliopo katika Halmashauri ya Mji Tarime una eneo lenye ukubwa wa ekari 266.65. Wananchi wanaozunguka eneo hilo walikuwa wakiutumia Mlima Nkongore kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi ikiwemo ukataji kuni, uchomaji mkaa na kilimo kinyume na taratibu za Mamlaka ya Upangaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Mlima Nkongore ni moja ya eneo lililokuwa limekithiri kwa shughuli haramu ikiwemo kilimo cha bangi. Hivyo, mwezi Novemba, 2017 Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Tarime ilikabidhi eneo hilo kwa Jeshi la Magereza ili kuhakikisha kuwa eneo hilo linalindwa kwa mujibu wa Sheria ya Mazingira Namba 20 ya mwaka 2004 kifungu cha 58(1) na (2) ambacho kinazuia kufanya shughuli zozote zinazoweza kusababisha hifadhi ya mlima kuharibiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Tarime kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais - Muungano na Mazingira inakamilisha taratibu za kulifanya eneo la Mlima Nkongore kuwa hifadhi. Hivyo, eneo la Mlima Nkongore litaendelea kuwa chini ya uangalizi wa Jeshi la Magereza hadi taratibu zitakapokamilika na kulitangaza kuwa eneo la hifadhi, ahsante.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI K.n.y. MOSHI S. KAKOSO Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya shilingi milioni 400 aliyoahidi Waziri Mkuu kuchangia katika ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kasekese kinachojengwa na wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuboresha utoaji wa huduma za afya ya msingi kwa wananchi ikiwemo upatikanaji wa huduma za upasuaji. Ujenzi na ukarabati huo unahusisha pia utekelezaji wa ahadi za Viongozi Wakuu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ya Serikali kuchangia shilingi milioni 400 ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kasekese imetekelezwa, ambapo fedha hizo zimepelekwa kwenye Kata ya Kasekese tarehe 25/8/2021 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo hicho.

Mheshimiwa Spika, majengo manne yanatarajiwa kujengwa, ambayo ni jengo la wodi ya wazazi, jengo la upasuaji, jengo la kufulia nguo na nyumba ya mtumishi. Aidha, ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje la Kituo cha Afya Kasekese umekamilika kwa gharama ya shilingi 164.9 kupitia fedha za mapato ya ndani ya Halmashauri. Ahsante sana.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia Wananchi wenye Viwanja eneo la Miganga West na East, Kata ya Mkonze katika Manispaa ya Jiji la Dodoma kwa kuwa uthamini ulishafanywa na baadhi ya Wananchi bado hawajalipwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifauatavyo:-

Mheshimiwa Spika, eneo la Miganga West na East katika Kata ya Mkonze ni miongoni mwa maeneo ya Halmashauri ya Jiji la Dodoma ambayo yamepangwa, kupimwa viwanja na kumilikishwa kwa wananchi ili waviendeleze kwa mujibu wa Mpango Kabambe wa Mji Mkuu (Master Plan).

Mheshimiwa Spika, kufuatia uwepo wa miradi ya kimkakati wa ujenzi wa reli ya kisasa (SGR) na ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa 400KV kutoka Chalinze hadi Zuzu inayotekelezwa na Serikali kupita katika eneo hili na kuathiri viwanja vilivyomilikishwa, imelazimu eneo hilo kutwaliwa chini ya Sheria ya Utwaaji Ardhi Na. 47 ya Mwaka 1967, Sheria ya Ardhi Na. 4 ya Mwaka 1999, Kanuni za Ardhi za Mwaka 2001, Miongozo ya Uthamini na Sheria ya Uthamini na Usajili wa Wathamini Na. 7 ya Mwaka 2016.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilifanya uthamini kwenye jumla ya viwanja 309 vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.77 vilivyoathiriwa na mradi wa reli ya kisasa ambapo kiasi cha shilingi milioni 576.5 imeshalipwa kwa wananchi ikiwa ni fidia ya viwanja 231. Viwaja 78 vyenye thamani ya shilingi bilioni 1.2 vinaendelea kuhakikiwa na Ofisi ya Mthamini Mkuu ili kukamilisha taratibu za fidia zao kwa mujibu wa sheria. Aidha, Serikali imeshafanya uthamini kwenye viwanja 123 na makaburi manne vyenye jumla ya thamani ya shilingi bilioni 1.1 vilivyoathiriwa na mradi wa ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa 400KV.

Mheshimiwa Spika, wananchi ambao viwanja vyao vimeathirika na mradi huo, watalipwa fidia mara baada ya Mthamini Mkuu kukamilisha taratibu za kisheria. Ahsante sana.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga Stendi ya Mabasi Makete Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga Mbunge wa Jimbo la Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Makete katika Mwaka wa Fedha 2013/2014 ilitenga eneo lenye ukubwa wa ekari 3.1 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha kisasa cha mabasi.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2014/ 2015 Halmashauri ilianza ujenzi kwa gharama ya shilingi milioni 40; na katika Mwaka wa Fedha 2022/2023 Halmashauri imepanga kutenga fedha kwenye mapato ya ndani ili kuendelea na ujenzi wa kituo hicho

Mheshimiwa Spika, Serikali inaishauri Halmashauri ya Wilaya ya Makete kufanya tathimini ya ujenzi wa kituo cha mabasi na kuandaa andiko ili kutafuta vyanzo vya fedha kwa ajili ya ujenzi. Ahsante sana.
MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatafuta mkakati wa kudumu wa kutatua tatizo la migogoro ya wakulima na wafugaji katika maeneo ya Mkoa wa Lindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tecla Mohamed Ungele, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Lindi kumekuwa na ongezeko la migogoro ya wakulima na wafugaji, hususan katika Wilaya za Kilwa, Nachingwea na Liwale. Migogoro hii imetokana na ongezeko la mifugo ambapo kumeongeza uhitaji wa nyanda za malisho na maji.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Sekretarieti ya Mkoa wa Lindi pamoja na Halmashauri ya Wilaya za Kilwa, Nachingwea na Liwale imefanya uhakiki na kubaini jumla ya migogoro 19, ambapo jumla ya migogoro 12 imetatuliwa na migogoro saba iko katika hatua mbalimbali za utatuzi.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Sekretariati ya Mkoa wa Lindi imeendelea kutekeleza mikakati mbalimbali ikiwemo kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi katika vijiji 81, na kuunda kamati ya utatuzi wa migogoro kwa kila halmashauri ili kuwahamasisha wafugaji kufuga kibiashara kwa kuendeleza ranch ndogondogo, na kila halmashauri kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kuandaa mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye vijiji vitano kila mwaka.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Halmashuri za Mkoa wa Lindi na kwa kushirikiana na wadau mbalimbali imepanga kutumia kiasi cha shilingi milioni 279.22 kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi kwenye vijiji 15, ikiwa ni hatua za utatuzi wa migogoro hiyo. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza:-

Jimbo la Lushoto lina Kituo kimoja cha Afya na sasa wananchi wameanza kujenga Vituo vya Afya viwili vya Gare na Ngwelo.

Je, Serikali ipo tayari sasa kutoa fedha kwa ajili ya kumalizia vituo hivyo na ni lini itafanya hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa za Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Jimbo la Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Lushoto kuanzia mwaka wa fedha 2017/ 2018 - 2019/2020, Serikali imetoa shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la wodi ya wazazi katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto pamoja na ukarabati na upanuzi wa Vituo vya Afya vya Mlola, Kangagai na Mnazi ili kuviwezesha kutoa huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Machi 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Lushoto shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maboma matatu ya zahanati. Serikali inatambua na kuthamini juhudi za wananchi wa Jimbo la Lushoto katika ujenzi wa Vituo vya Afya. Serikali itaendelea kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya nchini, vikiwemo vituo vya afya vilivyoanza kujengwa kwa nguvu za wananchi Jimboni Lushoto kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga stendi ya kisasa Jijini Arusha ili kukidhi mahitaji ya Wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Jiji la Arusha imetenga eneo lenye ukubwa wa ekari 30 katika eneo la Bondeni City kwa ajili ya ujenzi wa stendi mpya ya kisasa. Stendi mpya itakayojengwa itazingatia pia mahitaji ya wafanyabiashara wadogo kama Machinga, stendi ya teksi, pikipiki, bajaji, Ofisi za Polisi wa Usalama Barabarani na maeneo ya huduma mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi inayoendelea sasa ni taratibu za manunuzi kwa ajili ya kumpata Mhandisi Mshauri atakayefanya upembuzi yakinifu wa mradi huo. Mradi huu wa ujenzi wa Stendi ya Kisasa Jiji la Arusha utajumuishwa kwenye Mradi wa Uboreshaji Miundombinu yaani Tanzania Cities Transforming Infrastructures and Competitiveness - TACTIC utakaotekelezwa kwenye Halmashauri 45 za Majiji, Manispaa na Miji nchini ambapo Serikali inaendelea na majadiliano na Benki ya Dunia.
MHE. VICENT P. MBOGO aliuliza:-

Jimbo la Nkasi Kusini lina Kata 11 na Kituo cha Afya kimoja pekee:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza Vituo vya Afya hasa katika Tarafa ya Chala, Kate, Myula, Sintali na Ninde?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vincent Paul Mbogo, Mbunge wa Nkasi Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi, ambapo katika mwaka wa fedha 2017/2018 hadi mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imejenga na kukarabati Vituo vya Afya vya Nkomolo na Kirando kwa gharama ya shilingi milioni 900. Aidha, katika mwaka wa fedha 2018/2019, Serikali imetoa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi. Vilevile, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kusogeza zaidi huduma za afya kwa wananchi, Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi inakamilisha utaratibu wa kuingia makubaliano ya utoaji wa huduma za afya (service agreement) na Kituo cha Afya cha Mzimwa kinachomilikiwa na Taasisi ya Kikatoliki Abei kwa ajili ya wananchi kupata huduma za afya ikiwemo upasuaji wa dharura ambapo wananchi kutoka Tarafa za Myula na Sintali ni miongoni mwa watakaonufaika na mpango huo. Aidha, Halmashauri imetenga eneo katika Tarafa ya Chala kwa ajili ya kuanza ujenzi wa kituo cha afya kupitia fedha za mapato ya ndani katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kujenga na kupanua vituo vya kutolea huduma za afya katika Jimbo la Nkasi na nchini kote kwa awamu kwa kuwa shughuli hizi ni endelevu.
MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ununuzi wa Vifaa Tiba ikiwemo vya upasuaji katika Kituo cha Afya cha Mwabayanda Wilayani Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, Kituo cha Afya Mwabayanda kilipatiwa shilingi milioni 400 kwa ajili ya upanuzi kwa kuwa awali ilikuwa ni zahanati. Ujenzi na ukarabati wa Kituo cha Afya Mwabayanda umekamilika na kituo kimeanza kutoa huduma za dharura za upasuaji kwa akina mama wajawazito kuanzia mwezi Oktoba 2020 baada ya kupatiwa vifaa tiba kutoka kwenye vituo vingine vilivyopo katika Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mwaka wa Fedha 2020/2021, Serikali imetoa shilingi bilioni 26 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyojengwa awamu ya kwanza na ya pili na vifaa vya shilingi bilioni 15 tayari vimeshapokelewa na taratibu za kupeleka vifaa vya shilingi bilioni 11 zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya cha Mwabayanda kilijengwa katika awamu ya nne; na hivyo vituo vyote vya afya vilivyojengwa awamu ya tatu na ya nne vitatengewa fedha ya ununuzi wa vifaa tiba katika bajeti ya mwaka 2021/2022. Aidha, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Maswa kupitia mapato yake ya ndani itoe kipaumbele cha ununuzi wa vifaa tiba kwa awamu ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi wakati Serikali ikiendelea kutafuta fedha za ununuzi wa vifaa tiba.
MHE. GHATI Z. CHOMETE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Sera ya Matibabu Bure kwa Wazee wenye umri kuanzia miaka 60 katika Halmashauri za Mkoa wa Mara inatekelezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inatekeleza Sera ya Afya ya Mwaka 2007 na Sera ya Taifa ya Wazee ya mwaka 2003, inayoelekeza kutoa matibabu bila malipo kwa wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo kwa kuwatambua na kuwapatia huduma mbalimbali za afya. Hadi Desemba, 2020 jumla ya wazee 2,344,747 wametambuliwa sawa na asimilia ya 87 ya makadirio ya wazee wote nchini. Kati yao wanaume ni 1,092,310 na wanawake 1,252,437. Aidha, wazee wasiokuwa na uwezo 1,087,008 wamepatiwa vitambulisho vya matibabu bure na wazee 856,052 wamepatiwa kadi za matibabu ya Afya ya Jamii (ICHF).

Mheshimiwa Spika, hadi Februari, 2021 Halmashauri za Mkoa wa Mara zimefanya utambuzi wa wazee 70,170 kati ya lengo la kuwatambua wazee 196,000. Kati ya wazee waliotambuliwa, wanaume ni 32,900 na wanawake ni 37,270. Wazee 39,664 wamepewa vitambulisho vya matibabu kati ya wazee 70,170 waliotambuliwa.

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Mara na Mikoa mingine inaendelea kufanya utambuzi kwa wazee na kuhakikisha wazee wote wanaotambuliwa wanapewa vitambulisho vya matibabu bila malipo. Aidha, Serikali itaendelea kuwatambua wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo ili waweze kunufaika na Sera ya Matibabu Bila Malipo.
MHE. CHARLES M. KAJEGE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itazikarabati barabara za Jimbo la Mwibara ambazo zimeharibika sana ili kuruhusu mawasiliano kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Mugeta Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ina majimbo mawili ya Uchaguzi ambayo ni Bunda Vijijiini na Mwibara yenye mtandao wa barabara wenye urefu wa kilomita 527.55. Serikali imekuwa ikitenga fedha za matengenezo ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda ambapo katika mwaka wa fedha 2019/20 shilingi milioni 546.87 zilitumika kwa ajili ya matengenezo ya barabara na shilingi bilioni 708.56 zimeidhinishwa katika mwaka wa fedha 2020/21 kwa ajili ya matengenezo ya barabara katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda.

Mheshimiwa Spika, ili kuboresha miundombinu ya barabara katika jimbo la Mwibara katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali imefanya matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 28.2 na makalvati 11 kwa gharama ya shilingi milioni 237. 43. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/ 21 shilingi milioni 460.44 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara zenye urefu kilomita 54.5 na makalvati 29 ambapo utekelezaji unaendelea.

Mheshimwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha za ujenzi na matengenezo ya barabara za Wilaya ya Bunda na nchini kote kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA K.n.y. MHE. KATANI A. KATANI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunga mkono juhudi za wananchi wa Kata za Mnyawa, Nanhyanga, Nambahu, Kitama na Nguja ambao wameanza kujenga vituo vya afya kwa nguvu zao wenyewe kwa kutoa fedha ili kukamilisha ujenzi wa vituo hivyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Katani Ahmad Katani, Mbunge wa Tandahimba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kupitia mpango wa uboreshaji wa vituo vya kutolea huduma za afya ya msingi ulioanza katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Tandahimba shilingi milioni 400 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya Mahuta, ambapo ujenzi na upanuzi umekamilika na kituo kinatoa huduma ikiwemo ya upasuaji wa dharura.

Mheshimiwa Spika, mwezi Machi, 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Tandahimba shilingi milioni 150 kwa ajili ya kumalizia maboma ya zahanati nne za Miuta, Chikongo, Mnazi Mmoja na Mabamba. Vilevile, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imepanga kutumia shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati na shilingi milioni 500 zitatengwa katika mapato ya ndani kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya cha Kitama.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuunga mkono juhudi za wananchi kwa kutenga fedha za kukamilisha maboma ya zahanati, vituo vya afya na hospitali kwa awamu vikiwemo vituo vya afya katika Kata za Nanhyanga, Nambahu, Kitama na Nguja.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza:-

Serikali ilitoa shilingi 500,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Biharamulo, lakini kiasi cha shilingi 204,000,000 kilirejeshwa baada ya kufunga mwaka Julai, 2020.

(a) Je, ni lini fedha hizo zitarejeshwa ili ujenzi uendelee?

(b) Gharama ya ujenzi ni shilingi 1,500,000,000; je, ni lini kiasi cha shilingi 1,000,000,000 kitatolewa ili kukamilisha ujenzi wa hospitali hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo ilipatiwa shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali mpya ya Halmashauri ambapo majengo yaliyojengwa ni Jengo la Wagonjwa wa Nje na Maabara na majengo yote mawili yamefikia asilimia 80 ya ukamilishaji. Aidha, kati ya fedha hizo zilizotolewa shilingi milioni 204 zilirejeshwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali baada ya kuvuka mwaka wa fedha 2019/2020 kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti ya fedha ya mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2016.

(b) Mheshimiwa Spika, mwezi Januari 2021 Serikali imetoa shilingi bilioni 1 kwa Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo ili kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Majengo yatakayojengwa ni Jengo la Utawala na Jengo la Wazazi ambayo yamefikia asilimia 40 ya ukamilishaji, Jengo la kuhifadhia dawa na Jengo la kufulia ambayo yamefikia asilimia 60 ya ukamilishaji. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Hospitali hiyo imetengewa shilingi milioni 300.
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga na kukarabati majengo ya Hospitali ya Wilaya ya Mbinga kutokana na kukosa baadhi ya majengo na yaliyopo kuchakaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Mjini kama ifuatavyo;

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Mbinga ina majengo saba ambayo ni jengo la akinamama, jengo la huduma za Bima, jengo la upasuaji, jengo la maabara, jengo la kuhifadhia maiti, jengo la mionzi na jengo la wagonjwa wa nje. Baadhi ya majengo hayo yana uchakavu wa wastani na mengine yana uchakavu wa hali ya juu. Jengo muhimu linalokosekana katika hospitali hiyo ni jengo la wodi ya watoto. Serikali imefanya tathmini ya hali ya uchakavu wa miundombinu ya hospitali hiyo ili kuona namna bora ya kufanya ukarabati au ujenzi wa hospitali mpya ya halmashauri. Kuanzia Mwaka wa Fedha 2017/2018 hadi 2019/2020, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri imefanya ukarabati wa jengo la wodi maalum na jengo la wagonjwa wa nje kwa gharama ya shilingi milioni 45.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga na katika mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali imeipatia Halmashauri ya Mji wa Mbinga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya, Kalembo ambacho ukarabati wake umekamilika na huduma zinatolewa ikiwemo huduma za upasuaji. Aidha, mwaka 2021 Serikali imeipatia shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya Zahanati za Kagugu, Iringa na Ruwaita. Vile vile katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imeomba kuidhinishiwa shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa awamu itaendelea kujenga na kukarabati miundombinu ya kutolea huduma za afya nchini kote ikiwemo katika Halmashauri ya Mji wa Mbinga.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza:-

Je, ni lini Kituo cha Afya Kinesi kitapandishwa hadhi na kuwa Hospitali kamili kutokana na kituo hicho kuhudumia wananchi zaidi ya vijiji 27 katika Jimbo la Rorya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru, na kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Rorya katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali ilipatia Halmashauri ya Wilaya ya Rorya shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ambapo tayari ujenzi wa majengo saba ya awali umekamilika na huduma za wagonjwa wa nje zinatolewa.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu ambapo tayari Halmashauri imeshazipokea fedha hizo na fedha shilingi milioni 500 zimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali ya Halmashauri ya Rorya. Hivyo, Serikali haikusudii kupandisha hadhi Kituo cha Afya Kinesi kuwa Hospitali ya Halmashauri kwa kuwa Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Rorya shilingi milioni 900 kwa ajili ya kuboresha Kituo cha Afya Utegi kilichopewa shilingi milioni 500 na Kituo cha Afya Kinesi kilichopewa shilingi milioni 400 ambapo ujenzi na ukarabati wa vituo hivyo umekamilika na huduma za upasuaji zimeanza kutolewa. Aidha, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma matatu ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo kimoja cha afya wilayani Rorya na shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma matatu ya zahanati.
MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka vitendea kazi Kituo cha Afya Kata ya Mtii, Jimbo la Same Mashariki baada ya kukamilika kwa vyumba 12 vya Jengo la OPD?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuweka kumbukumbu sahihi kwanza naomba nianze kwa ufafanuzi kwamba jengo linalojengwa eneo la Mtii ni zahanati na si kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zahanati ya mpya inayojengwa kwa nguvu za wananchi, fedha za Mfuko wa Jimbo, wadau wa maendeelo pamoja na fedha za Halmashauri. Majengo yanayojengwa ni pamoja na Jengo la Wagonjwa wa Nje na Jengo la Huduma ya Kliniki ya Afya ya Mama na Mtoto ambayo tayari yamekamilika na ujenzi wa Jengo la Huduma za Uzazi unaendelea. Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Same imepokea fedha shilingi milioni 150 iliyotengwa kwenye bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021 ambapo Zahanati ya Mtii imepokea shilingi milioni 50 itakayotumika kukamilisha Jengo la Wazazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Zahanati ya Mtii itakapokamilika itapatiwa usajili na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto na kuwekewa utaratibu wa kupatiwa vitendea kazi.

Aidha, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele cha ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali za Halmashauri na Vituo vya Afya vilivyojengwa na kukarabatiwa na kote nchini, vikiwemo Vituo vya Afya vya Ndungu, Shengena na Kisiwani ambavyo vimepokea shilingi milioni 400 kila kimoja na Zahanati ya Kasapo iliyopokea shilingi milioni 154 vilivyoko kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Same ambavyo tayari vimepokea fedha hizo na shughuli za ujenzi zinaendelea ujenzi na ukarabati wa vituo hivyo umekamilika na huduma sasa zinatolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Same iweke kipaumbele kwa kutenga bajeti kwa kupitia mapato yake ya ndani kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vya zahanati mpya ya Mtii pindi itakapokamailika na kupatiwa usajili.
MHE. BONNAH L. KAMOLI aliuliza:-

(a) Je, ni lini Serikali itaongeza Vituo vya Afya katika Kata za Jimbo la Segerea Pamoja na kupandisha hadhi Zahanati za Kinyerezi, Segerea, Kipawa na Yombo Kiwalani ili kuondoa adha kwa wananchi wa Kata 13 wanaotegemea Kituo kimoja cha Afya?

(b) Je, ni lini Kata za Minazi Mirefu, Buguruni, Kimanga na Kisukuru zitapatiwa Zahanati?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bonnah Ladislaus Kamoli, Mbunge wa Segerea, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali iliipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam; iliyokuwa Halmashauri ya Manispaa ya Ilala shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Mwezi Februari 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tatu kwenye Hospitali ya Halmashauri na imeitenga shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2020/ 2021 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 na 2019/2020, Serikali iliipatia Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Guluka Kwalala na upanuzi wa Kituo cha Afya Buguruni.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam kupitia mapato yake ya ndani, imetenga shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vitatu vya afya na shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya kuongeza miundombinu katika zahati tano ili ziweze kupandishwa hadhi kuwa vituo vya afya zikiwemo Zahanati za Kinyerezi na Kiwalani katika Jimbo la Segerea.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 250 kwa ajili ya kukamilisha maboma matano ya zahanati katika Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam zikiwemo Zahanati za Bonyokwa na Tabata zilizopo katika Jimbo la Segerea. Aidha, kupitia mapato ya ndani, Halmashauri ya Jiji la Dar es Salaam imetenga shilingi bilioni 2.5 kwa ajili ya kulipa fidia kwenye maeneo ambayo yatachukuliwa na Serikali kwa ajili ya ujenzi na upanuzi wa vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Segerea na nchini kote ili kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza:-

Wananchi wa Kata ya Imalamate Wilayani Busega wamejenga zahanati na kumaliza maboma manne kwa maana ya zahanati moja kila kijiji:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi hao kuezeka maboma hayo ili waweze kupata huduma za afya kwenye zahanati hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya huduma za afya katika Wilaya ya Busega, ambapo katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukarabati wa Kituo cha Afya Nasa na kukiwezesha kuanza kutoa huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 Serikali iliipatia halmashauri hiyo shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Vilevile, mwezi Februari, mwaka 2021 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tati katika Hospitali ya Halmashauri na imetenga shilingi milioni 500 katika bajeti ya mwaka 2020/2021 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Februari, 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Ng’wang’wenge, Sanga na Mkula. Vilevile, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati ya Imalamate, Ijutu na Busami katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Busega na nchini kote ili kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza:-

Je, ni lini watumishi waliohamishiwa Halmashauri ya Uvinza kutoka Halmashauri ya Kigoma Vijijini watalipwa stahiki zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Kigoma Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya Uvinza ina watumishi 99 wanaostahili kulipwa stahiki za uhamisho kufuatia kuhamishwa kutoka Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma kwenda Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza katika mwaka wa fedha 2013/2014. Kiasi cha shilingi milioni 319.89 kinahitajika ili kulipa madeni hayo ya watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais – TAMISEMI imezielekeza Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza kuanza kutenga fedha kupitia mapato yake ya ndani kwa ajili ya kulipa madeni na stahili za watumishi. Aidha, Serikali itaendelea kuhakiki madeni ya watumishi na kuyalipa kwa kadri wa upatikanaji wa fedha.
MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa maboma ya vituo vya afya yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi katika Kata za Makuro na Ngimu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ili kuboresha huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida, katika mwaka wa fedha 2018/2019 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Singida shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, hospitali hiyo imetengewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wa wodi tatu na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati Minyeye, Mnung’una na Msikii katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 250 kwa ajili ya kukamilisha maboma matano ya zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida ili kuunga mkono jitihada zinazofanywa na wananchi katika kujenga na kuboresha miundombinu ya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Singida Kaskazini zikiwemo Kata za Makuro, Ngimu na nchini kote ili kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itarekebisha tatizo la Hospitali ya Frelimo ambayo inapata mgao kama Kituo cha Afya wakati ni Hospitali ya Wilaya ya Iringa tangu mwaka 2013?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Jonathani Msambatavangu, Mbunge wa Jimbo la Iringa Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vituo vya kutolea huduma za afya nchini ikiwemo Hospitali za Halmasahuri hupatiwa mgao wa fedha za ruzuku kwa ajili ya uendeshaji na ununuzi wa dawa na vitendanishi na vifaa tiba kwa kuzingatia vigezo maalum vilivyowekwa. Vigezo hivyo ni pamoja na idadi ya watu wanaopata huduma katika eneo husika, umbali kilipo kituo, pamoja na idadi ya vifo vya watoto chini ya miaka mitano katika Halmashauri husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, utofauti wa mgao baina ya vituo vya kutolea huduma za afya ikiwemo Hospitali ya Frelimo na Hospitali nyingine za Halmashauri hutokana na vigezo hivyo. Hospitali ya Manispaa ya Iringa Frelimo ilisajiliwa tarehe 25 Julai, 2013 kama Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa na ilianza kupokea mgao wa ruzuku ya fedha za uendeshaji kama Hospitali kuanzia Agosti, 2013 ambapo kwa mwaka huu wa fedha mpaka Machi imepokea kiasi cha shilingi 53,32.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu iliyopo katika Hospitali ya Frelimo ni pamoja na jengo la Utawala, jengo la Huduma za Wagonjwa wa Nje, jengo la huduma za Maabara, jengo la huduma za Mionzi, jengo la Ufuaji na jengo la Huduma za Afya ya Uzazi na Mtoto. Miundombinu inayokosekana katika Hospitali hii ni pamoja na jengo la upasuaji, Wodi za kulaza wagonjwa, jengo la kuhifadhia maiti, na jengo la kutunzia dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuongeza majengo kwenye Hospitali hii ili kuboresha huduma zinazotolewa. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya upungufu wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe hasa kwenye Idara za Afya, Elimu na Kilimo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – Tawala za Miko ana Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ikama ya mwaka 2020/2021, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe inapaswa kuwa na watumishi 2,630. Hadi Machi 2021 Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe ilikuwa na watumishi 2,294 hivyo ina upungufu wa watumishi 336 sawa na asilimia 12.8.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Ikama Idara ya Afya katika Halmashauri ya Wlaya ya Korogwe inapaswa kuwa na watumishi 392, na hadi Machi 2021 Idara ya Afya ilikuwa na watumishi 263 hivyo ina upungufu wa watumishi 129 sawa na asilimia 32.9. Idara za Elimu msingi na sekondari zinapaswa kuwa na watumishi 1891 lakini zina watumishi 1604 hivyo zina upungufu wa watumishi 287 sawa na asilimia 15.2. Idara ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika inapaswa kuwa na watumishi 55 na ina watumishi 45 hivyo ina upungufu wa watumishi 10 sawa na asilimia 18.2.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imeendelea kuajiri na kuwapnaga watumishi wa kada mbalimbali katika halmashauri nchini ambapo katika mwaka wa fedha 2020/21 watumishi 81 wapya waliajiriwa na kupangwa katika Halamshauri ya Wilaya ya Korogwe. Kati ya hao, watumishi 22 ni walimu wa sekondari, 35 shule za msingi, 6 watumishi wa kada za afya na Afisa Ugani 1 pamoja na 17 wa kada mbalimbali. Pamoja na jitihada hizo, katika Ikama ya mwaka 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya imetenga nafasi za ajira mpya 150 ambao watapangwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe.
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza:-

Je, Serikai haioni umuhimu wa kuajiri Wafamasia angalau katika kila Kituo cha Afya nchini ili kuimarisha usimamizi na mtiririko wa upatikanaji dawa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa ikama wa watumishi wa afya, Mfamasia anapaswa kuwepo katika ngazi ya Hospitali. Kwenye ngazi ya Vituo vya Afya na Zahanati, ikama inaelekeza kuwepo kwa Mteknolojia wa Dawa au Mteknolojia Msaidizi wa Dawa. Kada hizi ni muhimu kuwepo kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ili kuimarisha uratibu na usimamizi wa bidhaa za afya.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Mei, 2017 hadi Februari, 2021 Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeajiri Wafamasia 79, Wateknolojia wa Dawa 313 na Wateknolojia wa Dawa Wasaidizi 160. Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa Wataalam hawa, ambapo katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 imepanga kuajiri watumishi 10,467 wakiwemo Wafamasia na Wateknolojia wa Dawa watakaopelekwa kwenye Hospitali za Halmashauri, Vituo vya Afya pamoja na zahanati kote nchini.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza:-

Kumekuwa na changamoto ya huduma za Afya katika Zahanati zetu hasa ukosefu wa dawa pamoja na huduma bure kwa wazee, watoto na akinamama wajawazito.

Je, ni lini Serikali itahakikisha Sera ya Afya inatekelezwa bila tatizo lolote?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa dawa katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini kwa kuongeza bajeti ya dawa, vitendanishi na vifaa tiba kutoka shilingi bilioni 31 katika mwaka wa fedha 2015/2016 hadi shilingi bilioni 270 katika mwaka wa fedha 2020/2021. Ongezeko hilo la fedha limewezesha kuongeza upatikanaji wa dawa muhimu (tracer medicine) kutoka wastani wa asilimia 31 mwaka 2015/2016 hadi asilimia 90 kufikia Aprili 30, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Mei, 2021 Serikali imetoa huduma ya matibabu bila malipo yenye gharama ya shilingi bilioni 30.1 kwa wananchi wa makundi maalum milioni 12 ikijumlisha wazee, wajawazito na watoto wenye umri chini ya miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na jitihada hizi, bado kuna changamoto ya upatikanaji wa baadhi ya dawa za makundi maalum kama wazee, wajawazito na watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano. Ili kukabiliana na changamoto hiyo, mwezi Novemba, 2020 Serikali ilitoa shilingi bilioni 41.2, mwezi Februari, 2021 Serikali ilipeleka shilingi bilioni
18.2 katika vituo vya kutolea huduma za afya ngazi ya msingi kwa ajili ya ununuzi wa dawa na mwezi Mei, 2021 Serikali imepeleka shilingi bilioni 80 na kufanya jumla ya fedha zote zilizopelekwa kwa ajili ya dawa kufikia shilingi bilioni 140.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuboresha upatikanaji wa dawa na bidhaa nyingine za afya ili kuboresha huduma kwa makundi maalum na wananchi kwa ujumla.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya wanaume, akina mama na watoto katika Hospitali ya Wilaya ya Frelimo katika Manispaa ya Iringa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Ritta Enespher Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Iringa (Frelimo) imeanza kufanya kazi kama Hospitali ya Halmashauri mwezi Februari, 2012 na kusajiliwa rasmi mwaka 2013. Katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Manispaa ya Iringa shilingi milioni 400 kwa ajili ya upanuzi wa hospitali ambapo jengo la maabara na jengo la mionzi yalijengwa na kukamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, miundombinu iliyopo katika Hospitali ya Frelimo ni pamoja na jengo la utawala, jengo la huduma za wagonjwa wa nje (OPD), jengo la huduma za maabara, jengo la huduma za mionzi, jengo la kufualia na jengo la huduma za afya ya uzazi na mtoto. Miundombinu inayokosekana katika hospitali hii ni pamoja na jengo la upasuaji, wodi za kulaza wagonjwa, jengo la kuhifadhi maiti na jengo la kutunzia dawa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya watoto, wodi ya wanaume na wodi ya wanawake magonjwa mchanganyiko (medical ward).
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza:-

Je, ni kwa nini Hospitali ya Mji Tarime isipandishwe hadhi na kuwa Hospitali ya Kanda Maalum ya Tarime na Rorya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Mji Tarime ina Wodi nane na vitengo mbalimbali vya huduma ikiwemo maabara, jengo la mionzi, chumba cha upasuaji, huduma za mama na mtoto, chumba cha dawa, chumba cha magonjwa ya akili, macho, duka la dawa lakini pia miundombinu mingine. Hospitali hii inahudumia wastani wa wagonjwa 140 wa nje (OPD), lakini inahudumia wagonjwa 70 wanaolazwa kwa siku. Hospitali ina jumla ya vitanda 180.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kanda ya Ziwa tayari ina Hospitali ya Rufaa ambayo ni Hospitali ya Bugando iliyopo Mkoa wa Mwanza. Hivyo, Serikali haikusudii kuipandisha hadhi Hospitali ya Mji Tarime kuwa Hospitali ya Rufaa ya Kanda Maalum ya Tarime na Rorya. (Makofi)
MHE. NICHOLAS G. NGASSA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaipatia Hospitali ya Wilaya ya Igunga gari la kubebea wagonjwa kwa kuwa lililopo limechakaa sana?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicholas George Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, gari la wagonjwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Igunga ni chakavu na halifai kuendelea kutumika. Kwa sasa Hospitali ya Halmashauri ya Igunga imepatiwa gari la Kituo cha Afya kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Igunga kutoka katika Kituo cha Afya cha Choma ambalo linatoa huduma katika Hospitali ya Wilaya ya Igunga.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto za uchakavu wa magari ya kubebea wagonjwa katika Hospitali na Vituo vya Afya nchini. Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kununua magari ya kubebea wagonjwa na itatoa kipaumbele kwa Hospitali na Vituo vya Afya vyenye uhitaji mkubwa wa magari ya kubebea wagonjwa.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakipatia Kituo cha Afya cha Muyama Wilayani Buhigwe vifaa vya Ultrasound na X-ray?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Muyama katika Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe hakitoi huduma ya uchunguzi wa Ultrasound na X-ray kutokana na ukosefu wa majengo lakini na vifaa hivyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali inamuelekeza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Buhigwe kupanga kununua Ultrasound kupitia mapato ya ndani wakati Serikali Kuu inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kununua X-ray. Aidha, ikiwa mapato ya ndani ya Halmashauri hayatoshelezi, Serikali inamshauri Mkurugenzi kukopa kupitia NHIF na kununua mashine ya Ultrasound wakati Serikali inapanga kununua X- ray.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza:-

Je, Serikali ipo tayari kutenga fedha kwa ajili ya kumalizia ujenzi wa Vituo vya Afya vya Mwangozo na Uyowa katika Jimbo la Ulyankulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Jimbo la Ulyankulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2020/2021 imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua kiasi cha Shilingi milioni 600 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo cha Afya cha Uyowa na ujenzi unaendelea. Aidha, Serikali kwa kushirikiana na wananchi inaendelea na ujenzi wa Kituo cha Afya Mwangozo. Hadi Aprili 2021, shilingi milioni 158.69 zinazotokana na michango ya wananchi na mapato ya ndani ya halmashauri zimetumika kujenga jengo la wagonjwa wa nje na wodi ya wazazi ambapo ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021, halmashauri imetenga shilingi milioni 25 na katika mwaka wa fedha 2021/2022, Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua imetenga shilingi milioni 140 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi.
MHE. PRISCUS J. TARIMO aliuliza:-

Je, ni nini mpango wa Serikali kuwawezesha akina baba kiuchumi baada ya mpango wa Halmashauri wa kuwawezesha akina mama, vijana na watu wenye ulemavu kuwa na mafanikio makubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeendelea kuwezesha wananchi kiuchumi kwa kutoa mikopo isiyo na riba kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu. Mikopo hiyo hutolewa kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa, Sura 290 kifungu cha 37A inayoelekeza kutenga 10% ya mapato yanayokusanywa na Halmashauri kwa ajili ya mikopo ya 4% kwa wanawake, 4% kwa vijana na 2% kwa watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, lengo la mikopo hii ni kusaidia makundi maalum katika jamii ambayo hayawezi kupata mikopo katika mabenki ya biashara na taasisi za fedha kwa sababu ya masharti magumu ikiwemo dhamana na riba kubwa. Hivyo, Serikali ilitoa kipaumbele kwa makundi ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kwa kuwa wengi wao hawakopesheki katika mabenki na taasisi za fedha. Kwa sasa Serikali haikusudii kuanzisha mpango wa kuwawezesha wanaume au akina baba katika mikopo hii.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kwa sababu Hospitali iliyopo haikidhi mahitaji kutokana na uchakavu na ongezeko la watu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Jimbo la Manyoni kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa hospitali 43 kongwe na chakavu za Halmashauri ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni. Serikali inaendelea kufanya tathmini ya miundombinu ya hospitali hizo ili kuona namna bora ya kuziboresha ikiwemo kuzikarabati au kujenga hospitali mpya kulingana na matokeo ya tathmini.

Mheshimiwa Spika, Serikali imepanga kukamilisha kwanza ujenzi wa Hospitali za Halmashauri 28 na hivyo baada ya ujenzi huo kisha hospitali chakavu zitawekewa mpango.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itazirejesha fedha za ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Msalala zilizorudishwa na mfumo baada ya mwaka wa fedha 2019/2020 kuisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christina Christopher Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ilipatiwa shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Hadi Juni 30 mwaka 2020, Halmashauri hiyo ilikuwa imetumia shilingi milioni 22.4 pekee na hivyo shilingi milioni 477.59 zilirejeshwa kwenye Mfuko Mkuu wa Serikali kwa mujibu wa Sheria ya Bajeti Namba 11 ya Mwaka 2015 na Kanuni zake za mwaka 2015. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Msalala shilingi bilioni 1 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Msalala kwa awamu hadi ujenzi wa hospitali hiyo utakapokamilika.
MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italeta gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Mgololo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Mgololo kilipatiwa gari la kubeba wagonjwa mwaka 2018 ambalo linalotumika kwa sasa kuhudumia wagonjwa wa dharura kwenye kituo hicho. Hata hivyo, kutokana na udogo wa gari hilo na ugumu wa jiografia ya eneo husika, gari la kubebea wagonjwa lililopo Kituo cha Afya Kasanga hutumika kuhudumia wagonjwa wa dharura inapohitajika.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa magari ya kubebea wagonjwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na kwa kulizingatia hilo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Halmashauri imenunua gari ya wagonjwa kwa kutumia mapato yake ya ndani lenye thamani ya shilingi milioni 174.

Aidha, Halmashauri imefanya matengenezo ya magari mawili ya wagonjwa ambayo yalikuwa mabovu kwa muda mrefu na kufanya Halmashauri kuwa na jumla ya magari matano ya kubebea wagonjwa. Magari haya yanatumika kubeba wagonjwa mara tu dharura zinapotokea katika vituo vya afya vilivyopo Wilayani Mufindi.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ya wagonjwa ili kuboresha huduma za rufaa Wilayani Mufindi na nchini kwa ujumla, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati barabara zilizoharibika hasa barabara za vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua adha kubwa inayotokana na kuharibika kwa miundombinu ya barabara uliosababishwa na mvua nyingi zilizonyesha msimu wa mwaka 2019/2020 na msimu wa mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeongeza bajeti ya matengenezo ya barabara ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kutoka shilingi bilioni 275.03 iliyotengwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 hadi shilingi bilioni 400 iliyotengwa katika mwaka wa fedha 2021/2022 ambalo ni ongezeko la Shilingi bilioni 124.97 sawa na aslimia 45.4. Ongezeko hili litaiwezesha TARURA kufanya matengenezo ya miundombinu ilyoharibika kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti ya ujenzi na matengenezo ya barabara kadri ya upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara ya Igunga – Miswaki – Loya – Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida yenye urefu wa kilometa 89?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daudi Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Igunga – Miswaki –Loya – Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida ni barabara inayouganisha Wilaya za Igunga na Uyui. Kwa upande wa Wilaya ya Igunga, barabara hii inajulikana kama barabara ya Igunga – Itumba – Buhekela – Simbo na ina urefu wa kilometa 107. Kwa upande wa Wilaya ya Uyui barabra hii inaunganisha barabara tatu ambazo ni Simbo - Miswaki - Loya – Migongwa – Magulyati yenye urefu wa kilometa 72.8, hivyo kufanya urefu wa barabara ya Igunga – Miswaki – Loya –Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida kuwa na urefu wa kilometa 179.8.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA Halmashauri za Wilaya ya Igunga na Uyui zimetenga jumla ya shilingi milioni 361.99 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida, kilometa 27, maeneo korofi kilometa 8.7 na matengenezo maalumu kilometa tano na ujenzi unaendelea. Aidha, katika mwaka 2021/2022 TARURA Halmashauri za Wilaya ya Igunga na Uyui zimetenga jumla ya shilingi milioni 235 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida kilometa 35 na ujenzi wa daraja dogo (box culvert) mawili, makalvati mistari minne ili kuimarisha maeneo korofi ya barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kuzifanyia matengenezo barabara katika maeneo mbalimbali nchini kulingana na upatikanaji wa fedha, nashukuru sana.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza: -

Je, ni lini Hospitali ya Wilaya ya Rorya itaanza kutoa huduma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Jimbo la Rorya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya ambapo kati ya mwaka wa fedha 2018/2019 hadi 2020/2021 Serikali imeipatia shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tisa na shughuli za ujenzi zinaendelea ambapo ujenzi wa majengo saba ya awali umekamilika na tangu Juni 2020 inatoa huduma ya wagonjwa wa nje (OPD). Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba na katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Rorya.

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Rorya inatarajiwa kuanza kutoa huduma za upasuaji wa dharula na kulaza wagonjwa ifikapo Disemba, 2021.
MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Afya Bashnet baada ya Serikali ya Kijiji kutenga eneo kwa ajili ya ujenzi huo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Babati Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na mpango wa kuboresha utoaji wa huduma za afya kwa kuendelea na ujenzi wa vituo vya afya nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Babati. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya ya Babati kupitia mapato yake ya ndani imetenga shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Kituo cha Afya Bashnet katika eneo lenye ukubwa wa ekari 12.6 lililotengwa na Serikali ya Kijiji.

Mhjeshimiwa Spika, Ujenzi huo utaanza katika mwaka wa fedha 2021/2022 kama ilivyopangwa.
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kupeleka watumishi wa Idara ya Afya katika Jimbo la Kilwa Kaskazini ambalo lina uhaba mkubwa wa watumishi kiasi cha kufanya baadhi ya zahanati kutoa huduma duni na nyingine kuchelewa kufunguliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa ina jumla ya vituo vya kutolea huduma za afya 60 zikiwemo hospitali mbili, vituo vya afya vitano na zahanati 53. Katika kipindi cha kuanzia mwaka 2017 hadi Desemba, 2020, Serikali imeajiri na kuwapanga watumishi 108 wa kada mbalimbali za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa. Aidha, mwezi Mei, 2021 Ofisi ya Rais-TAMISEMI imetangaza nafasi 2,726 za ajira za kada mbalimbali za afya. Watumishi hao watapangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini kwa kutoa kipaumbele kwenye vituo vya kutolea huduma za afya vyenye upungufu mkubwa wa watumishi ikiwemo baadhi ya vituo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi wa kada mbalimbali za afya na kuwapangia katika vituo Wilayani Kilwa na kote nchini kwa ujumla, ahsante sana.
MHE. REGINA N. QWARAY aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka na kuongeza vifaa tiba na wataalam katika vituo vya afya ilivyojenga vikiwemo vifaa tiba maalum kama vile “incubator beds” na taa maalum kwa ajili ya kukabiliana na homa ya manjano kwa watoto njiti?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Regina Ndege Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika,utekelezaji wa mpango wa ujenzi wa vituo vya afya unaenda sambamba na mpango wa ununuzi wa vifaa tiba. Kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2020/2021 Serikali imetoa jumla ya Shilingi bilioni 68.7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika vituo vya afya vilivyojengwa na kukarabatiwa ili kuwezesha utoaji wa huduma za dharura na upasuaji kwa akinamama wajawazito na wananchi kwa ujumla. Vifaa vilivyonunuliwa vinajumuisha vifaa kwa ajili ya kusaidia watoto wanaozaliwa kabla ya muda (Infant Radiant Warmers).

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imetoa shilingi bilioni 34 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali mpya 67 za Halmashauri zilizojengwa kuanzia mwaka wa fedha 2017/ 2018.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Mei, 2017 hadi Mei, 2020 Serikali imeajiri na kuwapanga watumishi 9,531 wa kada mbalimbali za afya katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Aidha, mwezi Mei 2021 Ofisi ya Rais - TAMISEMI imetangaza nafasi 2,726 za kada mbalimbali za afya. Wataalam hao watapangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini na kipaumbele kitakuwa kwenye vituo vyenye uhitaji mkubwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha huduma za afya nchini kwa kuboresha miundombinu, kununua vifaa tiba na kuajiri wataalam wa kada mbalimbali za afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha, ahsante sana.
MHE. DAVID M. KIHENZILE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italeta gari la wagonjwa katika Kituo cha Afya cha Mgololo?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Mgololo kilipatiwa gari la kubeba wagonjwa mwaka 2018 ambalo linalotumika kwa sasa kuhudumia wagonjwa wa dharura kwenye kituo hicho. Hata hivyo, kutokana na udogo wa gari hilo na ugumu wa jiografia ya eneo husika, gari la kubebea wagonjwa lililopo Kituo cha Afya Kasanga hutumika kuhudumia wagonjwa wa dharura inapohitajika.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa magari ya kubebea wagonjwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na kwa kulizingatia hilo kwa mwaka wa fedha 2020/2021 Halmashauri imenunua gari ya wagonjwa kwa kutumia mapato yake ya ndani lenye thamani ya shilingi milioni 174.

Aidha, Halmashauri imefanya matengenezo ya magari mawili ya wagonjwa ambayo yalikuwa mabovu kwa muda mrefu na kufanya Halmashauri kuwa na jumla ya magari matano ya kubebea wagonjwa. Magari haya yanatumika kubeba wagonjwa mara tu dharura zinapotokea katika vituo vya afya vilivyopo Wilayani Mufindi.

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ya wagonjwa ili kuboresha huduma za rufaa Wilayani Mufindi na nchini kwa ujumla, ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati barabara zilizoharibika hasa barabara za vijijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emmanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Jimbo la Tabora Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua adha kubwa inayotokana na kuharibika kwa miundombinu ya barabara uliosababishwa na mvua nyingi zilizonyesha msimu wa mwaka 2019/2020 na msimu wa mwaka 2020/2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeongeza bajeti ya matengenezo ya barabara ya Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini (TARURA) kutoka shilingi bilioni 275.03 iliyotengwa katika mwaka wa fedha 2020/2021 hadi shilingi bilioni 400 iliyotengwa katika mwaka wa fedha 2021/2022 ambalo ni ongezeko la Shilingi bilioni 124.97 sawa na aslimia 45.4. Ongezeko hili litaiwezesha TARURA kufanya matengenezo ya miundombinu ilyoharibika kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti ya ujenzi na matengenezo ya barabara kadri ya upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara ya Igunga – Miswaki – Loya – Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida yenye urefu wa kilometa 89?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daudi Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Igunga – Miswaki –Loya – Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida ni barabara inayouganisha Wilaya za Igunga na Uyui. Kwa upande wa Wilaya ya Igunga, barabara hii inajulikana kama barabara ya Igunga – Itumba – Buhekela – Simbo na ina urefu wa kilometa 107. Kwa upande wa Wilaya ya Uyui barabra hii inaunganisha barabara tatu ambazo ni Simbo - Miswaki - Loya – Migongwa – Magulyati yenye urefu wa kilometa 72.8, hivyo kufanya urefu wa barabara ya Igunga – Miswaki – Loya –Migongwa – Magulyati hadi Iyumbu Singida kuwa na urefu wa kilometa 179.8.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 TARURA Halmashauri za Wilaya ya Igunga na Uyui zimetenga jumla ya shilingi milioni 361.99 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida, kilometa 27, maeneo korofi kilometa 8.7 na matengenezo maalumu kilometa tano na ujenzi unaendelea. Aidha, katika mwaka 2021/2022 TARURA Halmashauri za Wilaya ya Igunga na Uyui zimetenga jumla ya shilingi milioni 235 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida kilometa 35 na ujenzi wa daraja dogo (box culvert) mawili, makalvati mistari minne ili kuimarisha maeneo korofi ya barabara hiyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kujenga na kuzifanyia matengenezo barabara katika maeneo mbalimbali nchini kulingana na upatikanaji wa fedha, nashukuru sana.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je ni lini Serikali itaainisha mpaka kati ya Wilaya ya Mkalama na Hanang’ eneo la Singa na Limbadau ili kuondoa taaruki kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa kuna mgogoro wa mipaka ya Vijiji kati ya Wilaya za Mkalama na Hanang ambao umekuwepo kwa muda mrefu licha ya jitihada mbalimbali zilizochukuliwa na Serikali ikwemo vikao vya ujirani mwema baina ya wahusika wa mgogoro, Serikali ilitekeleza uwekaji wa alama za mipaka iliyotangazwa kwenye Gazeti la Serikali Na. 266 la tarehe 14 Desemba 1973 lililotangaza Wilaya ya Mbulu na Hanang’. Chanzo kikubwa cha mgogoro huo ni baaadhi ya wananchi kutokukubaliana na alama za mipaka zilizopo kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Namba 266 la uanzishwaji wa Wilaya ya Mbulu na Wilaya ya Hanang’.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri za Wilaya ya Hanang na Mkalama zimetenga jumla ya shilingi milioni 40 kwa ajili ya kupima Vijiji vya Singa na Limbadau ambavyo ndio vipo kwenye eneo la mgogoro. Serikali inatarajia mgogoro huo utamalizika, ahsante sana.
MHE. MWANTUMU M. ZODO K.n.y. MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Mtwara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara ambapo kuanzia mwaka wa fedha 2018/2019 hadi Mei, 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Hospitali hiyo inajengwa katika Kituo cha Afya Nanguruwe ambacho kitapandishwa hadhi kuwa Hospitali ya Halmashauri baada ya kuongeza miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi Mei, 2021 ujenzi wa majengo matano umekamilika. Ujenzi wa wodi tatu za kulaza wagonjwa unaendelea na unatarajiwa kukamilika mwezi Septemba, 2021. Aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika Hospitali ya Halmashauri. Vilevile katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua migogoro ya mipaka kati ya Vijiji vya Mwanholo na Nyenze dhidi ya Mwekezaji na Mchimbaji Madini Eli Hilal Wilayani Kishapu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nyangindu Boniphace Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mgogoro wa mipaka kati ya Vijiji vya Mwanholo na Nyenze dhidi ya Mwekezaji na Mchimbaji wa Madini aitwaye Eli Hilal Wilayani Kishapu unaohusisha eneo lenye ukubwa wa hekta 2,872.4. Eneo hilo awali lililkuwa linamilikiwa na Mgodi wa Wiliamson Diamond Limited, kabla ya kugawiwa kwa Mchimbaji Eli Hilal ambaye alimilikishwa na Serikali. Baadhi ya wanakijiji wa Mwanholo na Nyenze hawaitambui mipaka ya eneo la mwekezaji wa uchimbaji wa madini na wengine wanalalamikia maeneo yao kutwaliwa na mwekezaji wa uchimbaji bila kulipa fidia.

Mheshimiwa Spika, mwezi Februari, 2021, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga iliunda Timu ya Wataalam kwa ajili kufanya uchunguzi wa mgogoro huo. Timu iliyoundwa imewasilisha taarifa yake na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga inaendelea kuifanyia kazi taarifa iliyowasilishwa ili kubaini masuala yanayoweza kushughulikiwa na Mkoa na yale yanayohitaji uamuzi wa ngazi za juu. Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga itashirikiana na wananchi na wadau wote muhimu katika kutatua mgogoro huu na kuhakikisha haki inatendeka.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza:-

Halmasauri ya Wilaya ya Lushoto ina upungufu wa walimu wa shule za msingi takribani 1,270 kwa mujibu wa ikama: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka walimu katika Halmashauri hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, – TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha kuanzia mwaka wa fedha 2016/2017 hadi 2019/2020 Serikali imeajiri na kuwapanga walimu 148 wa shule za msingi na walimu 118 wa shule za sekondari katika Halmashauri ya Lushoto kati ya walimu 26,181 wa shule za msingi na sekondari walioajiriwa katika kipindi hicho. Aidha, Serikali inaendelea kuratibu zoezi la kuajiri walimu 6,949 kwa nafasi za ajira zilizotangazwa mwezi Mei, 2021 ambao watapangwa kwenye shule mbalimbali zikiwemo za Wilaya ya Lushoto, ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO K.n.y. MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutoa elimu ya ujasiriamali kwa wanawake na vijana katika Halmashauri wanapewa mikopo ya asilimia tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa Kanuni ya 23 ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo ya asimilia 10 kwa Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu za mwaka 2019, Mamlaka za Serikali za Mitaa zinapaswa kutoa mafunzo kwa vikundi vilivyokubaliwa kupata mikopo hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuzingatia Kanuni hiyo Serikali ilikwishaanza kutoa elimu ya ujasiriamali na katika mwaka wa fedha 2019/2020 Mamlaka za Serikali za Mitaa zimetoa mafunzo kwa vikundi 11,915 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ambavyo vilipewa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri zote nchini. Mafunzo yaliyotolewa ni pamoja na mafunzo ya ujasiriamali, utunzaji fedha, uendeshaji na usimamizi wa miradi, utoaji taarifa na usimamizi wa marejesho ya mikopo. Serikali kupitia Mamlaka za Serikali za Mitaa itaendelea kutoa elimu kwa vikundi hivyo ili kuvijengea uwezo wa kuendelea kukua na kutumia ipasavyo fursa mbalimbali za kiuchumi katika maeneo yao, ahsante.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza:-

Kituo cha Afya Upuge kinahitaji jengo kwa ajili ya mashine za mionzi yaani x-ray na ultra sound: -

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mashine hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Almas Athumani Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Uyui shilingi milioni 500 kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa Kituo cha Afya Upuge. Ujenzi wa majengo manne ulifanyika na majengo yote yanatumika. Serikali inatambua uhitaji wa jengo la x-ray na ultra sound katika kituo hicho. Serikali imekwishatoa ramani za majengo ya mionzi kwa Halmashauri zote nchini ikwemo Halmashauri ya Wilaya ya Uyui.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo, Serikali inaielekeza Halmashauri kutenga fedha za mapato ya ndani ili kuanza ujenzi huo kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha 2022/2023. Serikali itaendelea kuboresha majengo ya x-ray na ultra sound kote nchini.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza:-

Kituo cha Afya Msindo kilichopo Wilayani Namtumbo kinapata mgao mdogo wa dawa usiokidhi mahitaji: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza mgao wa dawa katika Kituo cha Afya Msindo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Msindo kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kilipandishwa hadhi kutoka Zahanati na kuwa Kituo cha Afya tarehe 26 Machi, 2014. Kituo hiki kimekuwa kikipokea mgao wa dawa kama Zahanati badala ya Kituo cha Afya kwa kuwa Halmashauri haikuwasilisha maombi husika kadri ya utaratibu. Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo imeendelea kuchukua hatua mbalimbali katika kukabiliana na changamoto hiyo ikiwemo kutumia fedha za makusanyo zinazotokana na uchangiaji wa huduma za afya kwa ajili ya ununuzi wa dawa. Wastani wa upatikanaji wa dawa muhimu katika kituo hiki ni asilimia 87.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kuwasilisha rasmi maombi ya mgao wa fedha za dawa za Kituo cha Afya Msindo kupitia ruzuku ya Serikali Kuu ili mgao huo urekebishwe na kukiwezesha kituo hicho kupatiwa mgao wa dawa wenye hadhi ya Kituo cha Afya, ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO aliuliza: -

Sekta ya Afya nchini ina upungufu wa Watumishi wapatao 16,000:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na changamoto hiyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA(MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa Sekta ya Afya nchini ina upungufu wa watumishi ambapo hadi mwezi Mei 2021 watumishi waliokuwepo ni asilimia 41 ya mahitaji halisi. Upungufu huo unatokana na sababu mbalimbali ikiwemo kustaafu kazi, kufariki na kuongezeka kwa idadi ya Vituo vya kutolea huduma za afya nchini kutokana na utekelezaji wa Programu ya Ujenzi na Ukarabati wa Vituo vya kutolea huduma za Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuanzia mwaka 2017 hadi 2020 Serikali kwa kushirikiana na wadau imeajiri watumishi 12,868 wa Sekta ya Afya ambao wamepangwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Adha, Serikali inakamilisha taratibu za ajira 2,726 za watumishi wa kada mbalimbali za afya zilizotangazwa Mwezi Mei 2021. Watumishi hao watapangwa kwenye Vituo vya kutolea huduma za afya vyenye uhitaji mkubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ili kukabiliana na changamoto hii, mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri watumishi wa kada za afya kwa awamu, nashukuru.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutekeleza Sera ya Afya ya kuwa na Kituo cha Afya kwa kila Kata ili kupunguza vifo vya Mama na Mtoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutekeleza Sera ya Afya ya kuwa na Zahanati kwa kila Kijiji na Kituo cha Afya kwa kila Kata kwa awamu ambapo kuanzia mwaka wa fedha 2015/2016 hadi 2020/2021 Serikali imejenga Zahanati 1,281, Vituo vya Afya 488 na Hospitali za Halmashauri 102. Mpango huu umewezesha kuongeza Vituo vya Afya katika Mamlaka za Serikali za Mitaa vyenye uwezo wa kutoa huduma za dharula za upasuaji kutoka Vituo 115 Disemba 2015 hadi Vituo 352 Juni 2021 na hivyo kuchangia katika kupunguza vifo vya mama wajawazito na Watoto. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali itaendelea na ujenzi wa vituo vya afya 121 na kiasi cha shilingi billioni 27.75 kimetengwa kwa ajili ya umaliziaji wa maboma 768 ya zahanati kote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkakati wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha za ujenzi wa vituo vya afya kwa awamu. Nakushukuru.
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza:-

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka uwiano sawa wa mikopo ya asilimia 10 inayotokana na mapato ya ndani bila kujali mapato ya halmashauri husika ili kusaidia wanufaika wa mikopo wanaoishi nje ya miji wapate fursa sawa na wanufaika wa mijini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, hutolewa kwa mujibu wa Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura ya 290 kifungu cha 37(a) na Kanuni zake za mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, msingi wa Sheria ya mikopo ya asilimia 10 ya wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu ni asilimia 10 ya Mapato ya Ndani ya Halmashauri baada ya kuondoa mapato lindwa. Hivyo kiwango cha mikopo kinatokana na uwezo wa makusanyo ya halmashauri husika. Halmashauri zimeelekezwa kutoa fursa sawa za mikopo kwa vikundi vyote vilivyokidhi vigezo vilivyopo ndani ya halmashauri husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo hii ni sehemu tu ya mifuko mbalimbali ya uwezeshaji wa wananchi kiuchumi iliyopo nchini, na Serikali itaendelea kuiboresha kadri itakavyohitajika.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Ofisi za Makao Makuu ya Halmashauri ya Sumbawanga katika Mji wa Laela baada ya agizo la Serikali la kuhamisha Makao Makuu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Jimbo la Kwela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ni miongoni mwa Halmashauri 30 zilizohamia kwenye maeneo mapya ya utawala mwaka 2019.

Mheshimiwa Spika, ili kuwezesha Halmashauri kutoa huduma bora kwa wananchi, Serikali imeweka mpango wa ujenzi wa jengo la utawala utakaogharimu shilingi bilioni 2.7.

Mheshimiwa Spika, mwezi Mei, 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuanza ujenzi. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuendelea na ujenzi huo. Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga imesaini mkataba wa ufundi na Chuo cha Sayansi Mbeya kwa ajili ya ujenzi utakaoanza tarehe 22 Juni, 2021.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha za ukamilishaji wa jengo hilo, ahsante sana.
MHE. HAWA M. CHAKOMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kurasimisha vitambulisho vya wajasiriamali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu Chakoma, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwezi Machi 2018, Serikali kwa kuwathamini na kuwajali wajasiriamali na watoa huduma wadogo ilianzisha utaratibu wa vitambulisho ili kuwawezesha kufanya biashara katika mazingira bora na tulivu zaidi. Vitambulisho hivi vilirasimishwa kutumiwa na wajasiriamali wenye mitaji yao na mauzo ghafi yasiyozidi shilingi milioni nne kwa mwaka.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka 2021 vitambulisho vya wajasiriamali wadogo vimefanyiwa maboresho kadhaa ikiwemo kuwekwa picha na jina la mjasiriamali mdogo aliyepatiwa kitambulisho hicho pamoja na ukomo wa muda wa kutumia kitambulisho hicho. Muda wa matumizi ni mwaka mmoja tangu tarehe ya kupatiwa kitambulisho badala ya mwaka wa kalenda kama ilivyokuwa awali.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuboresha vitambulisho vya wajasiriamali wadogo kadri itakavyohitajika, ahsante.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Kituo cha Afya Ikuwo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuboresha huduma za afya katika Wilaya ya Makete, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 400 katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Ipelele. Ujenzi wa Kituo hicho umekamilika na kinatoa huduma zikiwemo huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa Zahanati za Usungilo, Nungu na Matenga. Vilevile, Mei 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Makete shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Kitulo. Aidha, ombi la Kituo cha Afya Ikuwo limepokelewa na linafanyiwa tathimini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaipitia na kuiboresha Sera ya Ujenzi wa Zahanati kila Kijiji na Kituo cha Afya kila Kata ili ujenzi ufanyike kimkakati na kwa tija zaidi badala ya kila Kijiji na kila Kata. Ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itajenga Vituo vya Afya vya Issuna, Ikungi, Makiungu, Ntuntu na Misughaa ili kurahisisha huduma za dharura Wilayani Ikungi kwa kuwa Wilaya hii inapitiwa na Barabara ya Dodoma – Mwanza ambayo imekuwa na ajali za mara kwa mara?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka Gari la Wagonjwa ili kuwahisha majeruhi na wagonjwa katika Hospitali za Rufaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshmiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi iliyoanza kujengwa mwaka wa fedha 2018/2019 ambapo hadi mwezi Mei 2021 ilikuwa imepatiwa shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya ujenzi. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 800 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali hiyo. Hospitali hiyo itasaidia kuokoa maisha ya majeruhi wa ajali zitakazotokea eneo la Ikungi katika barabara ya Dodoma hadi Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 hadi Mei 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi shilingi milioni 900 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya Ihanja na Sepuka. Ujenzi wa Vituo hivyo umekamilika na vinatoa huduma ikiwemo huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inapitia Sera ya Zahanati katika kila Kijiji na Kituo cha Afya katika kila Kata na itafanyiwa maboresho yenye tija zaidi ili ili ujenzi uwe wa kimkakati badala ya kila Kijiji au kila Kata.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya Ikungi ina magari matatu ya kubebea wagonjwa ambayo yapo katika Vituo vya Afya Ikungi, Sepuka na Ihanja ambayo yote yanaendelea kutoa huduma za rufaa za dharura ndani na nje ya wilaya ya Ikungi. Ahsante.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE aliuliza: -

Je, Serikali imejipangaje kutatua changamoto iliyopo katika vituo vya kutolea huduma za afya ya kukosekana kwa Idara ya Huduma ya Mazoezi Tiba na Utengamao ukilinganisha na ongezeko la wagonjwa wanaohitaji aina hiyo ya tiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alice Karungi Kaijage, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa kuna ongezeko kubwa la uhitaji wa huduma ya mazoezi tiba na utengamao kwenye vituo vya kutolea huduma za afya, huku kukiwa na changamoto ya uwepo wa miundombinu stahiki, vifaa na wataalam kwenye vituo vingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imefanya tathmini ya mahitaji wa huduma ya mazoezi tiba na utengamao kwenye vituo vya kutolea huduma za afya na inaendelea kukamilisha mpango mkakati ambao utatoa mwongozo katika kutatua uhitaji wa huduma hizo. Ofisi ya Rais, TAMISEMI itatekeleza kikamilifu mpango utakaotolewa ili kuboresha huduma ya mazoezi tiba na utengamao katika vituo vya afya. Ahsante.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza: -

Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio itatambuliwa rasmi na kuanza kuwahudumia wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana na kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Jimbo la Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tangazo la kuanzishwa kwa Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio lilitolewa tarehe 1/10/2007 na Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa, Mamlaka za Wilaya Sheria Na. 7 ya mwaka 1982 kifungu cha 16 na 17.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2012/2013 Serikali iliunda timu ya wataalam kwa ajili ya kuchukua maoni ya wananchi kuufanya Mji Mdogo wa Nansio kuwa Halmashauri ya Mji. Wananchi wa kata kumi zilizopendekezwa kuunda Halmashauri ya Mji Nansio waliridhia Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio kupandishwa hadhi na kuwa Halmashauri ya Mji na mapendekezo hayo yaliwasilishwa Ofisi ya Rais-TAMISEMI na Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais-TAMISEMI ilipokea mapendekezo hayo na kutuma timu ya wataalam kwenda katika Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio ili kujiridhisha kama vigezo muhimu vinavyotakiwa ili kupandisha hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio vimefikiwa. Timu ilibaini kuwa Mamlaka ya Mji Mdogo Nansio bado haikidhi vigezo vya kupandishwa hadhi na kuwa Halmashauri ya Mji.

Mheshimiwa Spika, vigezo zilivyokosekana ni pamoja na kutokuwa na idadi ya watu angalau 150,000, kutokuwa na eneo lenye ukubwa wa walau kilomita za mraba 300, kutokuwa na kata walau 12 na mitaa 60. Hivyo, Ofisi ya Rais- TAMISEMI iliishauri Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe kuendelea kuilea Mamlaka ya Mji Mdogo wa Nansio mpaka itakapokidhi vigezo. Ahsante sana.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza: -

Wananchi wa Wilaya ya Same bado wanaendelea kutaabika sana kwa kukosa huduma bora za afya kwenye Hospitali ya Wilaya licha ya ahadi ya Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa ya ujenzi wa hospitali mpya ya Halmashauri ya Wilaya ya Same.

Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa ikizingatiwa kuwa eneo la ujenzi wa hospitali hiyo tayari limeshatengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Jimbo la Same Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya nchini zikiwemo Hospitali za Halmashauri. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni 55.7 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali 68 za Halmashauri zilizoanza kujengwa katika mwaka wa fedha 2018/2019. Pia Serikali imetenga shilingi bilioni 11.4 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali 27 za Halmashauri zilizoanza kujengwa katika mwaka wa fedha 2019/2020 na shilingi bilioni 14 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali 28 za Halmashauri katika Halmashauri 28 ambazo hazikuwa na Hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa Hospitali kongwe 43 za Halmashauri ambazo zina uchakavu wa miundombinu ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Same. Kupitia Programu ya Ujenzi na Ukarabati wa Vituo vya Kutolea Huduma za Afya nchini; Hospitali hizo zitaanza kujengwa upya kwa awamu kuanzia mwaka wa fedha 2022/ 2023. Ahsante.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba ikiwemo x-ray pamoja na vifaa vingine vya kupima wagonjwa katika hospitali zilizojengwa hivi karibuni hasa katika Wilaya mpya ikwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetoa shilingi bilioni 34 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali 67 za Halmashauri zilizoanza kujengwa katika mwaka wa fedha 2018/2019. Fedha hizo zimepelekwa Bohari Kuu ya Dawa na utaratibu za kupeleka vifaa tiba katika Hospitali 67 zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe Shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali mpya ya Halmashauri.

Aidha, mwezi Mei, 2021 Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe shilingi bilioni moja kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali ambapo majengo mapya matano yamejengwa na yameyakamilika. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa Hospitali na shilingi milioni 487 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Mbogwe. Ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO aliuliza: -

Je, ni lini mradi wa ujenzi wa soko la kisasa katika Halmashauri ya Mji wa Tarime wenye thamani ya shilingi bilioni 8.07 utakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Nicholas Matiko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji wa Tarime ilikidhi vigezo vya kupatiwa Shilingi bilioni 8.07 kwa ajili ya ujenzi wa soko la kisasa kupitia utaratibu wa Miradi ya Kimkakati mwezi Februari, 2019. Kutokana na changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa miradi ya kimakatati Serikali ilisitisha baadhi ya miradi ya kimkakati iliyoidhinishwa ukiwemo mradi wa ujenzi wa soko la kisasa katika Halmashauri ya Mji wa Tarime. Hata hivyo, Serikali imetoa kibali kwa Halmashauri ya Mji Tarime kuendelea na ujenzi wa Soko na katika mwaka wa fedha 2021/2022, shilingi bilioni tatu zimetengwa kwa ajili ya ujenzi wa soko katika Mji wa Tarime.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Mji Tarime inatarajia kutangaza kazi ya ujenzi wa soko la kisasa mwezi Julai, 2021 na ujenzi unatarajiwa kuanza mwezi Agosti, 2021 baada ya kumpata mkandarasi. Halmashauri imejipanga kukamilisha mradi huo ndani ya miezi 12 tangu tarehe ya kusaini mkataba.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia na kufanikisha kutoa namba kwa Vijiji vya Chipunda Kata ya Namatutwe, Mkalinga Kata ya Chikunja na Sululu ya Leo Kata ya Namatutwe vyenye Wakazi zaidi ya elfu kumi katika Jimbo la Ndanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Jimbo la Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, namba za usajili wa vijiji hutolewa kupitia Hati za Usajili wa Vijiji kwa kuzingatia matakwa ya Kifungu cha 22 na 26 cha Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya), Sura ya 287. Aidha, Vijiji hivyo hupaswa kuwa vimetangazwa kupitia Gazeti la Serikali kama ilivyoainishwa katika Kifungu cha 30 cha Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Wilaya) Sura ya 287.

Mheshimiwa Naibu Spika, Chipunda na Mkalinga ni Vitongoji katika Kijiji cha Namatutwe na Napata na Sululu ya Leo ni eneo ndani ya Kitongoji cha Maleta katika Kijiji cha Namatutwe, Kata ya Namatutwe katika Halmashauri ya Wilaya ya Masasi, hivyo maeneo hayo hayatambuliki kama Vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wakazi wa maeneo hayo wameonesha uhitaji wa kuanzisha Vijiji ni vema wakaanzisha kusudio la kuyafanya maeneo hayo kuwa vijiji kwa kuzingatia sheria pamoja na Mwongozo wa Uanzishaji Maeneo ya Utawala wa Mwaka 2014 kupitia mikutano na vikao kwenye ngazi ya vijiji, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya, Kamati ya Ushauri ya Mkoa na Ofisi ya Rais-TAMISEMI. Ahsante.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA K.n.y. MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Watumishi pamoja na vitendea kazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto ya upungufu wa watumishi, mwezi Julai, 2021, Serikali ilipeleka watumishi 28 wakiwemo watumishi 19 wa Sekta ya Afya na watumishi tisa wa Sekta ya Elimu. Aidha, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022, imepanga kuajiri jumla ya watumishi 477 ili kupunguza changamoto ya upungufu wa watumishi. Pamoja na jitihada hizo, Serikali itaendelea kufanya msawazo wa watumishi katika Halmashauri zote ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kwa kadri ya mahitaji.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa vitendea kazi, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni imetenga na kuidhinishiwa bajeti ya shilingi milioni 705.85 kwa ajili ya ununuzi wa vitendea kazi ikiwemo samani za ofisi pamoja na magari manne kwa gharama ya shilingi milioni 430.00. Mpaka sasa, Halmashauri ipo katika hatua za mwisho za ununuzi wa magari mawili ya awali kwa gharama ya shilingi milioni 220.00 yatakayosaidia kupunguza changamoto ya upungufu wa magari. Kwa ujumla, Serikali itaendelea kununua vitendea kazi kwa ajili ya halmashauri hiyo kulingana na upatikanaji wa fedha. Ahsante sana.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Gari la Wagonjwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali kupitia fedha za Mkopo wa Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF) imetenga shilingi bilioni 46.94 kwa ajili ya ununuzi wa magari ya wagonjwa 253, ambapo magari 195 yenye thamani ya shilingi bilioni 35.1 yatanunuliwa kwa ajili ya halmashauri zote 184, ambapo kupitia magari hayo Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi itapatiwa gari moja la wagonjwa. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Jengo la Wodi za kulaza Wagonjwa pamoja na kupeleka mashine ya X-ray katika Kituo cha Afya Itobo kilichopo Jimbo la Bukene?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jumanne Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imepeleka shilingi milioni 250 katika Kata ya Itobo kwa ajili ya ujenzi wa majengo ya kituo hicho ili kiweze kuwa na uwezo wa kutoa huduma za upasuaji. Ujenzi wa majengo hayo umeanza na unatarajiwa kukamilika ifikapo 30 Aprili, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa vituo hivi vya afya unafanyika kwa awamu. Hivyo, baada ya awamu hii ya kwanza ya ujenzi kukamilika, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa majengo mengine ikiwemo wodi katika Kituo cha Afya cha Itobo. Aidha, mashine za X-ray zitaendelea kununuliwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. MRISHO S. GAMBO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Wenyeviti wa Serikali za Mitaa wanapata malipo kama Madiwani na Wabunge kutokana na majukumu mazito wanayoyafanya ikiwemo ufuatiliaji wa malipo ya Kodi ya Majengo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua na kuthamini kazi kubwa inayofanywa na Wenyeviti wa Serikali za Mitaa, Vijiji na Vitongoji kwa kuwa ndio wasimamizi wakuu wa shughuli zote za maendeleo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni za Uchaguzi wa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa ngazi ya Vijiji na Mitaa za Mwaka 2014 chini ya Tangazo la Serikali Na. 322, miongoni mwa sifa zinazomwezesha mkazi wa Kijiji, Mtaa au Kitongoji kuchaguliwa kuwa Mwenyekiti ni pamoja na kuwa na shughuli halali inayomwingizia kipato.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa mwongozo kwa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhusu malipo ya posho ya viongozi hawa kwa kutumia mapato ya ndani kadri ya uwezo wa Halmashauri. Kwa ujumla, uwezo wa Halmashauri zilizo nyingi bado ni mdogo katika kutekeleza jukumu hili. Hivyo, Serikali imeichukua changamoto hii na itaendelea kufanya tathmini. Ahsante.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Zahanati na Vituo vya Afya katika Wilaya ya Kakonko?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati na Vituo vya vya Afya vya kimkakati nchini, ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni 38.15 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 758 kote nchini. Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko imetengewa shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati tatu.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa fedha za makato ya tozo za miamala ya simu shilingi bilioni 55.25 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya 221 kwenye Tarafa zisizo na Vituo vya Afya vyenye uwezo wa kutoa huduma ya upasuaji, ambapo Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko imepokea shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Tarafa ya Nyaronga kata ya Gwalama.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea kujenga zahanati na vituo vya afya katika Wilaya ya Kakonko na nchini kote katika maeneo ya kimkakati kulingana na vigezo vilivyowekwa badala ya kila Kijiji na kila Kata. Ahsante.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro uliopo mpakani mwa Wilaya ya Kishapu Kata ya Mwamalasa Kijiji cha Magalata na Wilaya ya Iramba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Jimbo la Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa, upo mgogoro wa mipaka kati ya Wilaya ya Kishapu na Wilaya ya Iramba. Mgogoro huo upo katika eneo la Bonde la Mto Manonga katika Kijiji cha Magalata Wilaya ya Kishapu na Kijiji cha Mwasangata Wilaya ya Iramba.

Mheshimiwa Spika, Mgogoro huu unatokana na malisho ya mifugo na maji, ambapo kwa upande wa Wilaya ya Kishapu jamii ya wafugaji wanaoishi kijiji cha Magalata hutumia bonde la Mto Manonga kwa ajili ya malisho na maji na upande wa Wilaya ya Iramba jamii ya wafugaji wanaoishi kijiji cha Masangata hutumia pia bonde la mto Manonga kwa ajili ya malisho na maji. Mgogoro huu mara nyingi hutokea wakati wa kiangazi ambapo jamii za pande zote mbili hutafuta malisho na maji kwa ajili ya mifugo ambayo hupatikana kwa wingi katika Bonde hilo.

Mheshimiwa Spika, vikao mbalimbali vya usuluhishi vimefanyika vikihusisha viongozi wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Uongozi wa Mikoa, Wilaya na Wananchi wa Vijiji vinavyohusika. Aidha, vikao hivyo vimesaidia kurejesha amani, utulivu na usalama kati ya vijiji hivyo hususan Magalata na Mwasangata.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea na jitihada za kuutatua mgogoro huu kwa njia shirikishi ili kudumisha amani na utulivu katika maeneo hayo. Ahsante.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Zahanati ya Ihalula kuwa Kituo cha Afya baada ya kukidhi vigezo vyote kwa muda mrefu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Philip Mwanyika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali iliipandisha hadhi zahanati ya Ihalula kuwa Kituo cha Afya mwaka 2018/2019 na kupewa namba ya utambulisho 101604-7. Aidha, Serikali katika mwaka wa fedha 2017/2018 ilipeleka Shilingi Milioni 500 kwa ajili ya ukarabati wa majengo mengine likiwemo jengo la upasuaji ambalo sasa linatoa huduma.

Mheshimiwa Spika, Kituo hiki kimekuwa kikilipwa fedha za Mfuko wa Bima ya afya kama zahanati kutokana na baadhi ya taratibu ambazo zilikuwa hazijakamilika.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto zimekwishalifanyia kazi na barua rasmi itapelekwa ndani ya mwezi huu. Ahsante.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuziwajibisha halmashauri nchini ambazo zinajiweza kimapato lakini hazipeleki asilimia 40 ya mapato ya ndani kwenye shughuli za maendeleo kama zinavyotakiwa kwa mujibu wa sheria na badala yake zimekuwa zikiwalazimisha wananchi wake wachangie?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Ranwell Mwenisongole, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwongozo wa Uandaaji wa Bajeti unaotolewa kila mwaka na Serikali unatoa maelekezo kwa halmashauri zote nchini kutenga sehemu ya mapato ya ndani kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo. Halmashauri zenye mapato yasiyolindwa chini ya shilingi bilioni tano zinapaswa kutenga asilimia 40 ya mapato ya ndani na Halmashauri zenye mapato yasiyolindwa zaidi ya shilingi bilioni tano zinapaswa kutenga asilimia 60 ya mapato ya ndani kwa ajili ya miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020 kiasi cha fedha shilingi bilioni 216.4 kimetumika kwenye shughuli za maendeleo sawa na asilimia 70.87 ya fedha zilizopaswa kutumika kwenye miradi ya Maendeleo.

Mheshimiwa Spika, aidha, katika mwaka wa fedha 2020/2021 kiasi cha shilingi bilioni 279.7 kimetumika kwenye miradi ya maendeleo sawa na asilimia 92 ya fedha zilizopaswa kupelekwa kwenye miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwisha wachukulia hatua watumishi 63 wakiwemo Wakurugenzi na Wakuu wa Idara, kwa kushindwa kutekeleza maagizo haya na utaratibu huu ni endelevu.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa rai kwa Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha Maelekezo haya yanatekelezwa kwa ufanisi. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza agizo la Rais wa Awamu ya Tatu la kuitambua Kizengi kuwa Tarafa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MITAA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala hufanyika kwa mujibu wa mwongozo wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala wa mwaka 2004.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mwongozo huu unaelekeza maombi ya kuanzisha maeneo hayo kujadiliwa na kupitishwa kwenye vikao vya kisheria ngazi za Vijiji, Kata (WDC), Wilaya (DCC) na Mkoa (RCC) kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais, TAMISEMI haijapokea maombi ya Kizengi kuwa Tarafa. Hivyo, naishauri Halmashauri ya Wilaya ya Uyui kufuata mwongozo uliotolewa na kuwasilisha maombi hayo Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya tathmini na kufanya maamuzi kwa kadri ya taratibu. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mhe. Waziri Mkuu aliyoitoa mwaka 2018 ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Kilombero?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga Mbunge wa Kilombero kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa Hospitali za Halmashauri nchini kote. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa hospitali 102 na kuanza ujenzi wa hospitali mpya kwenye halmashauri 28 zikiwemo hospitali zilizoahidiwa na viongozi wa kitaifa.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Ifakara ni miongoni mwa halmashauri 28 zisizo na Hospitali za Halmashauri, ambayo imetengewa fedha shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa majengo matatu ya awali. Ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. GHATI Z. CHOMETE Aliuliza: -

Je, ni lini agizo la Mheshimiwa Rais la kuboresha stendi ya Bweri Musoma Mjini litatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kujibu swali kwa ridhaa yako naomba nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu Mwingi wa Baraka kwa kutujaalia afya njema sisi sote na kutuwezesha kuendelea na majukumu haya ya kuwatumikia watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitumie fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa imani kubwa aliyonipa na kuteua kuendelea kuwatumikia watanzania wenzetu katika dhamanahii muhimu ya Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Naomba kumuahidi Mheshimiwa Rais kwamba nitafanya kazi kwa bidii yangu yote ili kuhakikisha imani yake na maono wake ya kuwatimizia maendeleo watanzania yanatimia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maelezo ya utangulizi, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, stendi ya mabasi ya Bweri katika Manispaa ya Musoma ilijengwa mwaka 2007 kwa mapato ya ndani ya halmashari kwa kutumia Mkandarasi CMG Construction Company Ltd aliyeingia mkataba wa shilingi bilioni 1.36 ambapo Mkandarasi huyo alifanya kazi zenye thamani ya shilingi milioni 921.17.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa stendi hiyo yenye uwezo wa kuingiza magari 35 hadi 45 ina miundombinu iliyochakaa hivyo inahitaji kuboreshwa. Kwa kutambua umuhimu wa stendi hiyo, tayari Halmashauri ya Manispaa ya Musoma imeandaa andiko la mradi huo na limewasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa ajili ya Uchambuzi wa kutengewa fedha kwa ajili ya ujenzi kupitia ufadhili wa Benki ya BADEA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utaratibu wa kupata ufadhili huo ili mradi huo pamoja na miradi mingine inayotarajiwa kutekelezwa kupitia ufadhili huo utekelezaji wake uweze kuanza. Ahsante.
MHE. SEIF K. S. GULAMALI Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais kutoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya Kata ya Ziba Wilayani Igunga aliyoitoa wakati wa Kampeni za uchaguzi 2020?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISMEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif K. S. Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kujenga Vituo vya kutolea Huduma za Afya katika Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuboresha utolewaji wa Huduma ya Afya ya Msingi kwa Wananchi. Ujenzi na Ukarabati wa Vituo unahusisha utekelezaji wa ahadi za viongozi kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika kutekeleza mkakati huu Serikali imepeleka kiasi cha shilingi bilioni 58.25 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vituo vipya vya afya 233 katika Tarafa na Kata za kimkakati ambazo hazikuwa na miundombinu hiyo. Aidha, Serikali imepeleka shilingi milioni 250 katika Halmashauri ya Wilaya ya Igunga kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya katika Kata ya Ziba ambapo ujenzi umefikia hatua ya umaliziaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mkakati huu Serikali itaendelea kutoa fedha katika Halmashauri kwa ajili ya utekelezaji wa ahadi za viongozi za kujenga au kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya kwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. HUSSEIN N. AMAR Aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi katika Vituo vya Afya vya Kharumwa na Nyang’hwale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nassor Hussein Amar, Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kuboresha upatikanaji wa watumishi wa kada za Afya katika Vituo vya kutolea huduma za Afya ili kuendana na upanuzi wa miundombinu ya Afya ya Msingi nchini. Katika Mwaka wa Fedha 2021/2022 Serikali iliajiri watumishi 2,726 wa kada mbalimbali za Afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika ajira hizo za Serikali, Halmashauri ya Wilaya ya Nyang’hwale ilipangiwa watumishi 20 ambapo Kituo cha Afya Kharumwa kilipata watumishi 3 na Kituo cha Afya Nyang’hwale kilipata watumishi 4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuajiri na kugawa watumishi kwenye Halmashauri na Vituo vya kutolea huduma za Afya kadri ya upatikanaji wa vibali vya ajira na fedha ili kuboresha utoaji huduma kwa wananchi.
MHE. FLORENT L. KYOMBO K.n.y. MHE. ELIBARIKI I. KINGU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza maboma ya Zahanati ya Ufana, Kinyampembe, Mpeti, Misake, Mlandala, Kaugeri na Mtavira ambayo yamejengwa kwa nguvu za wananchi kwa zaidi ya miaka mitano sasa katika Jimbo la Singida Magharibi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Elibariki Immanuel Kingu, Mbunge wa Singida Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kujenga vituo vya kutolea huduma za afya kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa ili kuboresha utoaji wa huduma za afya ya msingi kwa wananchi ikiwemo ukamilishaji wa maboma ya zahanati. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 28.2 za ruzuku kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 564 katika Halmashauri zote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hadi kufikia Disemba, 2021 tayari Serikali imepeleka shilingi bilioni 15.4 katika Halmashauri nchini kwa ajili ya utekelezaji wa bajeti iliyopangwa ambapo kati ya fedha hizo kiasi cha shilingi milioni 200 kimepelekwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kutekeleza ukamilishaji wa maboma ya zahanati nne za Ufana, Kinyampembe, Misule na Makotea. Aidha, Halmashauri kutumia mapato ya ndani imetenga shilingi milioni 50 kukamilisha boma la zahanati ya Kaugeri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeweka mpango wa kukamilisha ujenzi wa maboma ya zahanati yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi. Aidha, Serikali inazielekeza Halmashauri zote nchini kuendelea kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati hizo ili ziweze kutoa huduma tarajiwa kwa wananchi, ahsante.
MHE. ALLY J. MAKOA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara muhimu ya Iboni – Bolisa – Gubalisa iliyopo katika Halmashauri ya Mji wa Kondoa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Juma Makoa Mbunge wa Jimbo la Kondoa Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya Iboni – Bolisa – Gubalisa iliyopo Halmashauri ya Mji wa Kondoa yenye urefu wa kilometa 14.7 inaunganisha maeneo muhimu ya kiuchumi na ni barabara mbadala ya kuingia na kutoka mjini kwa wananchi wanaoelekea Kondoa Vijijini pamoja na Wilaya ya Jirani ya Babati.

Mheshimiwa Spika, barabara hii ina mahitaji ya vivuko vitano na daraja moja ambapo tathmini na usanifu umebainisha kuwa ujenzi wake utagharimu jumla ya shilingi bilioni 2.15. Utekelezaji wa kazi hii umepangwa kufanyika katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023 kwa kujenga vivuko na kuiwekea changarawe ili kuiwezesha kutoa huduma katika kipindi chote cha mwaka.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa mpango wa kuiwekea lami haujaandalliwa kutokana na ufinyu wa bajeti.
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. ERIC J. SHIGONGO Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itarejesha Mamlaka kwa Madiwani ya kuzisimamia halmashauri zao pamoja na kuwaazimia Wakurugenzi wa Halmashauri pale linapotokea tatizo kwenye halmashauri husika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eric James Shigongo, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mamlaka za ajira na nidhamu kwa Watumishi wa Halmashauri hutofautiana kwa mujibu wa Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 8 ya mwaka 2002 na Kanuni zake za mwaka 2003. Kwa mujibu wa Sheria hii Mamlaka ya nidhamu ya Wakurugenzi wa Halmashauri za Majiji ni Katibu Mkuu Kiongozi na Mamlaka ya nidhamu ya Wakurugenzi wa Halmashauri za Manispaa, Miji na Wilaya ni Waziri mwenye dhamana ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, halmashauri kupitia Baraza la Madiwani imepewa Mamlaka ya kusimamia nidhamu ya watumishi wengine wote wa halmashauri wakiwemo Wakuu wa Idara kwa kuzingatia kifungu cha 6 (6) cha Sheria ya Utumishi wa Umma Namba 8 ya mwaka 2002 na Kanuni zake za Mwaka 2003.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia Sheria hizo Waheshimiwa Madiwani hawana Mamlaka ya kuwawajibisha Wakurugenzi, ikitokea tatizo katika utendaji wa Mkurugenzi wa Halmashauri wanapaswa kutoa taarifa kwa Mamlaka husika. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha Makao Makuu ya Tarafa za Basotu, Endasak na Balangdalah kunajengwa Vituo vya Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang’, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kujenga vituo vya afya katika Tarafa na Kata za kimkakati ambapo, katika mwaka wa fedha 2020/2021 jumla ya shilingi bilioni 58.25 zimepelekwa kujenga vituo vya afya 233 kote nchini.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 Halmashauri ya Hanang’ ilipokea shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Tarafa ya Simbalay Kata ya Gisambalang na ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Hanang’ kupitia mapato ya ndani wametenga na kutoa kiasi cha Shilingi milioni 400 kwa ajili ya kuendelea na upanuzi wa Kituo cha Afya Bassotu. Aidha, kiasi cha shilingi milioni 500 kimtengwa katika mwaka 2022/2023 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Endasak.

Mheshimiwa Spika, Ujenzi wa vituo vya afya katika Halmashauri unajumuisha fedha za mapato ya ndani na maelekezo mahususi yametolewa kwa halmashauri zote nchini kutenga fedha za ujenzi wa vituo ili kuboresha huduma kwa wananchi. Ahsante.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI aliuliza: -

Je ni lini Serikali itapeleka Watumishi wa kada ya Ualimu na Afya katika Wilaya ya Lushoto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua mahitaji ya walimu na watumishi wa kada ya afya nchini kote ikiwemo Wilaya ya Lushoto. Wilaya ya Lushoto ina upungufu wa walimu kwa asilimia 44.4 na watumishi wa kada ya afya kwa asilimia 66.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali iliajiri watumishi 9,675 katika kada za afya na uwalimu ambapo Wilaya ya Lushoto ilipelekewa walimu 86 na watumishi wa kada ya afya 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la ajira ni endelevu na Halmashauri ya Lushoto itapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa vifaa tiba na dawa za kutosha kwenye vituo vya afya na zahanati zote katika Halmashauri ya Wilaya ya Msalala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Jimbo la Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuboresha upatikanaji wa dawa na vifaatiba, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali ilitenga shilingi bilioni 11.3 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na vifaatiba ambapo Halmashauri ya Msalala imetengewa shilingi milioni 376 kati ya fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala katika kipindi cha Mwaka wa Fedha 2021/2022, imetenga bajeti ya dawa na vifaatiba kiasi cha shilingi bilioni 1.5 ambapo hadi kufikia Desemba, 2021 kiasi cha shilingi milioni 403.2, sawa na asilimia 38.1 kimetolewa.

Aidha, Kituo cha Afya Isaka na Mwalugulu vimetengewa vifaa vya jumla ya shilingi milioni 600 na Zahanati za Matinje, Mwakima na Kabondo zimetengewa jumla ya shilingi milioni 150 kwa ajili ya vifaa na vifaatiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na Serikali Kuu, halmashauri zimeelekezwa kuimarisha na kudhibiti makusanyo ya fedha za uchangiaji wa huduma za afya ili kuhakikisha vifaatiba na dawa vinapatikana ipasavyo. Ahsante.
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA aliuliza: -

Je, Serikali haioni kuwa kuajiri Walimu bila kujali muda wa kuhitimu, baadaye baadhi yao watashindwa kuajiriwa kutokana na umri wao kuwa mkubwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Conchesta Leonce Rwamlaza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2020/2021 iliajiri Walimu wa shule za msingi na sekondari wapatao 6,949.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha haki inatendeka katika ajira hizo, Serikali ilitumia mfumo wa kielektroniki (Online Teachers’ Employment Application System – OTEAS) kwa ajili ya kupokea, kuchakata na kuwapangia vituo kwa mujibu wa vigezo vilivyowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya vipaumbele vya ajira hizo ni cha wahitimu waliohitimu miaka ya nyuma zaidi. Katika ajira hizo takribani asilimia 75.6 ni wahitimu kati ya mwaka 2014 hadi 2017 na wachache, takribani asilimia 24.4, ni wahitimu waliohitimu kati ya mwaka 2018 hadi 2019 ambao wengi walikuwa na mahitaji maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kuajiri Walimu kwa kuzingatia mwaka wa kuhitimu ambapo waliohitimu muda mrefu watapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaajiri Walimu wa Sayansi katika Shule za Sekondari za Kata Wilaya ya Temeke pamoja na kumaliza tatizo la uhaba wa Vifaa vya Maabara kwenye shule hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Temeke, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali katika Mwaka wa Fedha 2020/2021 iliajiri Walimu 6,949 ambapo kati yao asilimia 79 walikuwa Walimu wa sayansi ambao walipangiwa vituo katika Shule za Sekondari za Serikali, kipaumbele kikiwa ni shule zenye upungufu mkubwa kulingana na mahitaji ya wakati huo. Serikali imefanya tathmini ya mahitaji ya Walimu wa sayansi katika shule za sekondari na kubaini kuwa Manispaa ya Temeke ina upungufu wa Walimu wa Sayansi 631, sawa na asilimia 71.05 ya mahitaji. Serikali itaendelea kuajiri Walimu wa fani zote na kuwapangia vituo kulingana na mahitaji ya shule za sekondari zote nchini, zikiwemo Shule za Sekondari za Manispaa ya Temeke.

(b) Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/ 2021, Serikali ilinunua na kusambaza vifaa vya maabara katika Shule za Sekondari za Kata zipatazo 1,258 nchini zikiwemo shule 14 Manispaa ya Temeke ili kuwafanya wanafunzi waweze kujifunza kwa vitendo masomo ya Sayansi. Serikali kwa kushirikiana na Wadau wa Maendeleo ya Elimu nchini itaendelea kununua na kusambaza shuleni vifaa vya maabara katika shule za sekondari nchini, zikiwemo Shule za Sekondari za Manispaa ya Temeke. Ahsante.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamalizia ujenzi wa soko la ujirani mwema katika Kijiji cha Mukarazi ikiwemo miundombinu na ujenzi wa Kituo cha Forodha cha Pamoja katika Jimbo la Muhambwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Folrence George Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Soko la Mukarazi ulianza kutekelezwa Juni, 2018 na kukamilika Oktoba, 2020. Ujenzi wa Soko hilo umegharimu kiasi cha shilingi milioni 442.61 na kwa sasa soko limekamilika kwa asilimia 100 na linatumika mara mbili kwa wiki.

Mheshimiwa Spika, ili kufanya soko hilo kutumika kikamilifu Halmashauri imetoa kiasi cha Shilingi milioni 5.6 kwa ajili ya kupima viwanja 145 katika eneo la soko kwa ajili ya matumizi mbalimbali ikiwemo biashara, huduma za polisi na forodha. Ahsante.
MHE. NICODEMUS H. MAGANGA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia Wananchi Pori la Kanegere kwa matumizi ya Wafugaji kwa kuwa Pori hilo limepoteza sifa ya kuwa Hifadhi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Henry Maganga, Nicodemus, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe, kama ifatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Pori la Kanegere lina ukubwa wa hekta 725.24 na lipo kwenye Kijiji cha Kanegere ambacho kina eneo lenye ukubwa wa hekta 4,443.35. Kijiji hicho tayari kimeandaa Mpango wa Matumizi ya Ardhi kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi ya Kijiji Na.5 ya mwaka 1999 na Sheria ya Matumizi Ardhi Na.6 ya Mwaka 2007.

Mheshimiwa Spika, Pori la Kanegere linamilikiwa na kijiji na sehemu kubwa ya pori hilo ipo katika safu ya milima. Eneo hilo halifai kwa ajili ya shughuli za ufugaji kwani ni eneo lenye miinuko mikubwa ya milima.

Mheshimiwa Spika, kupitia Mpango wa Matumizi ya Ardhi ulioandaliwa, wananchi wamelitenga eneo hilo kwa ajili ya kuhifadhi na kupunguza mmonyoko wa udongo unaoathiri mazingira ya kijiji kwa ujumla wake. Aidha, kwa upande wa wafugaji mpango huo umetenga eneo la malisho lenye ukubwa wa hekta 405.02 ambalo inashauriwa wafugaji kulitumia kwa ajili ya mifugo yao.

Mheshimiwa Spika, hivyo, natoa wito kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe kushirikiana na Mamalaka husika ili kukamilisha taratibu za pori hilo kutangazwa rasmi kwenye Gazeti la Serikali kwa manufaa mapana ya Kijiji, Halmashauri na nchi kwa ujumla. Ahsante.
MHE. COSTANTINE J. KANYASU aliuliza: -

Je, nini kinakwamisha ujenzi wa stendi mpya ya Geita Mjini na lini sasa ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Constantine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi kwenye eneo la ukubwa wa hekta
6.9 unaendelea na upo katika hatua ya usanifu ambapo unafanyika pamoja na usanifu wa miradi mingine ya ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami nzito zenye urefu wa kilometa 15.4.

Mheshimiwa Spika, kazi za ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi imepangwa kuanza mwaka wa fedha 2022/2023, baada ya kukamilika kwa usanifu. Mradi huu umepangwa kutekelezwa na Serikali kupitia Mkopo wa Benki ya Dunia. Ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza: -

Je, ni lini Vituo vya Afya vya Nagaga na Mnavira vitakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Jimbo la Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018 Serikali iliipatia Halmashauri ya Masasi shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Nagaga ambapo ujenzi umekamilika na huduma zimeanza kutolewa.

Mheshimiwa Spika, aidha, Halmashauri ya Masasi katika mwaka wa fedha 2021/2022, imetenga shilingi milioni 23 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa nguzo na paa kwenye njia za watembea kwa miguu (walkways).

Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka 2009 hadi 2018 kiasi cha Shilingi milioni 110 kilitumika kwa ajili ya ukamilishaji wa boma la OPD la zahanati ya Mnavira. Kati ya fedha hizo shilingi milioni 68 zilitolewa na Serikali na shilingi milioni 42 nguvu za wananchi. Ujenzi wa jengo hilo la Zahanati ya Mnavira umekamilika na huduma zinaendelea kutolewa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022, shilingi milioni 500 zimepelekwa Halmashauri ya Masasi kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Chikoropola na Chikundi ambapo ujenzi wa vituo hivi unaendelea. Ahsante.
MHE. HAMIDA M. ABDALLAH aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Lindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamida Mohamed Abdallah, Mbunge wa Jimbo la Lindi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali mpya ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi. Mara baada ya kukamilika kwa ujenzi huo na kuanza kutoa huduma, miundombinu ya Hospitali ya Rufaa ya sasa itakuwa Hospitali ya Halmashauri ya Manispaa ya Lindi.

Mheshimiwa Spika, ili kuendelea kuimarisha na kuboresha huduma za afya kwa wananchi Serikali tayari imekwishaipatia Halmashauri ya Manispaa ya Lindi, shilingi milioni 500 kwa ajili ya kujenga kituo cha afya kwenye eneo la Kimkakati na lenye mahitaji makubwa. Ahsante. (Makofi)
MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupunguza uhaba wa watumishi katika Idara ya Elimu katika Mkoa wa Lindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tecla Mohamedi Ungele, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais -TAMISEMI ilifanya tathmini ya mahitaji ya walimu katika shule za msingi na sekondari nchi nzima na kubaini kuwa Mkoa wa Lindi unauhitajii jumla ya walimu wa shule za msingi 4,760 na waliopo ni 3,544 ikiwa ni upungufu wa walimu 1,216 sawa na asilimia 25.5 ya mahitaji. Kwa upande wa shule za sekondari, Mkoa wa Lindi unahitaji walimu 4,580 na waliopo ni 1,682 na upungufu ni walimu 2,898 sawa na asilimia 63.3 ya mahitaji.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hiyo nchini kote Serikali imetoa maelekezo kwa Wakurugenzi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa nchini kuhakikisha wanafanya msawazo wa walimu katika maeneo yao.

Pili, Serikali inakamilisha muongozo wa walimu wa kujitolea, utakaotumika kuwapata walimu wanaojitolea katika shule zenye uhitaji mkubwa. Walimu hao wanaojitolea watatambulika rasmi kupitia mfumo wa kielektroniki kwa ajili ya kupata chanzo sahihi cha kurejea utendaji kazi wao.

Tatu, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Ofisi ya Rais – TAMISEMI imeomba kibali cha kuajiri walimu 10,000 katika shule za msingi na sekondari nchini ikiwemo Mkoa wa Lindi. Ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU K.n.y. MHE. VINCENT P. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Boti ya kubebea Wagonjwa katika vijiji zaidi ya saba vilivyopo Mwambao mwa Ziwa Tanganyika katika Jimbo la Nkasi Kusini ambavyo havina huduma ya Zahanati wala Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vicent Paul Mbogo, Mbunge wa Jimbo la Nkasi Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti; Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga shilingi bilioni 35.1 kwa ajili ya ununuzi wa magari ya wagonjwa 195 ambayo yatapelekwa kwenye Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Nkasi Kusini. Aidha, Serikali imekwishapeleka fedha shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya King’ombe kwenye Kata ya Kala ambapo ujenzi unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Halmashauri ya Nkasi imetenga shilingi milioni 23 kwa ajili ya kufanya matengenezo ya magari ya kubebea wagonjwa na Boti zinazotoa huduma ili kuboresha na kuimarisha huduma kwa wagonjwa. Ahsante.
MHE. JANEJELLY J. NTATE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawalipa posho ya masaa ya ziada Watumishi wa afya waliofanya kazi kubwa sana katika kuokoa maisha ya Watanzania wakati wa mlipuko wa ugonjwa wa Covid-19?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Janejelly James Ntate, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilitoa maelekezo kwa Mamlaka za Mikoa na Halmashauri kuandaa madai yote ya posho za masaa ya ziada wanazodai Watumishi wa Afya waliofanya kazi katika mapambano ya kukabiliana na janga la ugonjwa wa UVIKO-19. Serikali ilipokea na kuhakiki madai yaliyowasilishwa ambapo kiasi cha shilingi bilioni 3.44 ndicho kinachostahili kulipwa ikiwa ni stahili kwa watumishi na wazabuni. Kati ya madai hayo, kiasi cha shilingi bilioni tatu sawa na 87% tayari zimepelekwa kwa ajili ya kulipa madeni hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wowote taratibu za kifedha zitakapokamilika, madeni na stahili za watumishi na wazabuni zilizosalia zitalipwa. Aidha, nazielekeza Mamlaka za Mikoa na Halmashauri waliopelekewa fedha za madeni hayo wazisimamie na kuhakikisha kila mtumishi anapata stahiki yake. Ahsante.
MHE. BONIVENTURA D. KISWAGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kuanzisha Wilaya mpya ya Kisesa Mkoani Mwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniventura Destery Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Magu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mwanza uliwasilisha mapendekezo ya kuanzisha Wilaya ya Bujora (Kisesa) kupitia barua ya tarehe 15 Machi, 2021 na tarehe 10 Mei, 2021. Ofisi ya Rais – TAMISEMI inaendelea na uchambuzi wa mapendekezo ya kuanzisha wilaya hiyo na maeneo mengine ya utawala yaliyowasilishwa. Uchambuzi wa taarifa hizo utakapokamilika timu ya wataalam itatumwa kufanya uhakiki na baadae kuishauri mamlaka ipasavyo juu ya suala hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge na wananchi wawe na subira katika kipindi ambacho Serikali inaendelea na uchambuzi na tathmini ya taarifa zilizowasilishwa.
MHE. REUBEN N. KWAGILWA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga miundombinu ya kisasa katika mnada wa Nderema?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Reuben Nhamanilo Kwagilwa, Mbunge wa Jimbo la Handeni Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali ilitenga kiasi cha Shilingi 287,194,890 kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi na uboreshaji wa miundombinu katika mnada wa mifugo wa Nderema uliyopo Halmashauri ya Mji wa Handeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mzabuni ameshapatikana na ameshakabidhiwa mradi mwezi Januari, 2022 na sasa ujenzi umeshaanza. Mradi huo unatarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2022 kwa mujibu wa mkataba.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kuigawa Wilaya ya Kilolo kuwa na Halmashauri mbili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Justin Lazaro Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mchakato wa kuanzisha eneo la utawala la wilaya unafanyika kwa Mujibu wa Sheria, Kanuni na kwa kuzingatia mwongozo wa kuanzishwa maeneo mapya ya utawala wa mwaka 2014. Aidha, maombi ya kuanzisha wilaya mpya yanatakiwa kujadiliwa na kupitishwa kwenye Vikao vya Kisheria ngazi ya Vijiji, Kata, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Kamati ya Ushauri ya Mkoa. Maombi hayo yanawasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya uchambuzi na uhakiki na baadaye kuishauri mamlaka ipasavyo juu ya suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Iringa haujawasilisha mapendekezo yanayohusu kugawa Wilaya ya Kilolo ili kuwe na Halmashauri mbili. Napenda kumshauri Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Kilolo kufuata utaratibu uliolekezwa hapo juu, ahsante.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI aliuliza: -

Je, Serikali inaweza kutoa tathmini ya urejeshwaji wa mikopo inayotolewa na Halmashauri kwa Vikundi vya Akinamama, Vijana, na Watu Wenye Ulemavu katika kipindi cha angalau miaka mitatu iliyopita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Stephen Kimei, Mbunge wa Jimbo la Vunjo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2018/2019, ilitoa mikopo kiasi cha shilingi bilioni 42.06 ambacho kiasi cha shilingi bilioni 12.88 kilirejeshwa sawa na aslimia 3.6; Mwaka wa fedha 2019/2020 kiasi cha shilingi bilioni 40.73 kilitolewa ambapo kiasi cha shilingi bilioni 14.65 kilirejeshwa sawa na asilimia 35.96; na katika mwaka wa fedha 2020/2021 kiasi cha shillingi bilioni 53.81 kilitolewa ambapo shilingi bilioni 29.85 kilirejeshwa sawa na asilimia 55.47.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshasanifu mfumo wa kieletroniki utakaowezesha usimamizi madhubuti wa mikopo katika usajili wa vikundi, utengaji wa fedha, utoaji wa mikopo, usimamizi wa marejesho na shughuli za vikundi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Aidha, mwongozo wa usimamizi wa mikopo hii umeshaandaliwa na upo kwenye hatua za mwisho za uidhinishaji.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kiwango cha mkopo wa 10% kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilianzisha utaratibu wa kutoa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri kwa vikundi vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu ili kusaidia makundi haya kuendasha shughuli zao za ujasiriamali na kujiongezea kipato.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali haijaweka mpango wa kuongeza asilimia ya mikopo hiyo. Aidha, tathmini ya kina inafanyika ili kubaini mafanikio na changamoto zilizopo ili hatua stahiki zichukuliwe katika kuboresha mikopo hiyo.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Vituo vya Afya eneo la Nsemulwa na Mwamkulu katika Manispaa ya Mpanda?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2021/ 2022 Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda imetenga fedha kiasi cha shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Nsemulwa ambapo hadi kufikia Februari, 2022 shilingi milioni 250 zimeshatolewa. Ujenzi wa majengo matatu ya wagonjwa wa nje, maabara na wodi ya wazazi unaendelea.

Mheshimiwa Spika, Serikali imepeleka fedha shilingi milioni 250 katika Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Mwamkulu ambapo ujenzi wa jengo la OPD umefikia hatua ya lenta na maabara umefikia hatua ya umaliziaji.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la upungufu wa wataalamu wa afya hasa ma-nurse katika Vituo vya Afya na Zahanati Mkoani Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Christine Gabriel Ishengoma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali iliajiri watumishi 2,726 wa kada mbalimbali za afya na kuwapeleka kwenye Halmashauri zote 184 ambapo Mkoa wa Morogoro ulipata jumla ya watumishi 156 ambao walipelekwa katika zahanati, vituo vya afya na hospitali.

Mheshimiwa Spika, mpango wa Serikali ni kuendelea kuajiri wataalam wa afya na kuwapeleka vituoni nchini kote. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kumalizia maboma yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi kwa ajili ya elimu, afya na polisi?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venant Daud Protas, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uwepo wa maboma 1,715 ya zahanti na vituo vya afya yaliyoanzishwa kwa nguvu za wananchi ambayo yanahitaji jumla ya shilingi bilioni 98.7 kwa ajili ya ukamilishaji wake. Aidha, katika sekta ya elimu kuna jumla ya maboma 12,101 ambayo yanahitaji jumla ya shilingi bilioni 183.5 kwa ajili ya ukamilishaji wake.

Mheshimiwa Spika, katika Bajeti ya mwaka 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni 43.8 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati na vituo vya afya ambapo hadi kufikia Desemba, 2021 shilingi bilioni 29.5 zimepelekwa kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma hayo. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/22 Serikali imetenga shilingi bilioni 79 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa na maabara ambapo fedha hizo tayari zimekwishapelekwa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi bilioni mbili kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vituo vya polisi 63 vilivyoanzishwa na wananchi kwa ajili ya kuimarisha huduma za usalama wa raia na mali zao katika maeneo yao ambapo hadi kufikia Desemba, 2021 shilingi bilioni 1.85 zimekwishatolewa sawa na asilimia 85. Mkakati wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha kwa awamu. Ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Hospitali ya Wilaya ya Mpwapwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi bilioni 16.55 kwa ajili ya kufanya ukarabati mkubwa wa hospitali kongwe za Halmashauri 19 kote nchini. Hospitali ya Halmashauri ya Mpwapwa ni miongoni mwa Hospitali hizo ambapo imetengewa Shilingi milioni 900 kwa ajili ya kazi hiyo. Ahsante.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA K.n.y. MHE. ALAUDIN H. SALIM aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali mpya ya Wilaya ya Ulanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Alaudin Hasham Salim, Mbunge wa Jimbo la Ulanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ulanga ina Hospitali ya Wilaya Ulanga ambayo ni kongwe na chakavu. Serikali itafanya tathmini ya hospitali hiyo ili kufanya maamuzi ya kuikarabati katika bajeti ya mwaka 2023/2024 au kuweka mpango wa kujenga hospitali mpya. Ahsante.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaigawa Kata ya Katumba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe Mbunge wa Jimbo la Nsimbo kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Spika, Serikali inatambua uhitaji wa kuigawa Kata ya Katumba kutokana na ukubwa wake na idadi kubwa ya watu.

Mheshimiwa Spika, kutokana na kuwepo kwa maeneo mengi ya utawala ambayo bado hayana miundombinu muhimu ya kiutawala na ya huduma za jamii, Serikali kwa sasa imeweka kipaumbele zaidi katika kujenga miundombinu hiyo ili kutoa huduma bora kwa wananchi badala ya kuanzisha maeneo mapya ya utawala.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo inashauriwa kukamilisha hatua za maombi na kuwa na subira katika kipindi hiki mpaka hapo Serikali itakapoona inaweza kuigawa Kata hiyo. Ahsante sana.
MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la kubebea wagonjwa katika Kituo cha Afya Gidas?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua uhitaji mkubwa uliopo wa magari ya kubebea wagonjwa kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 imefanya manunuzi ya magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatapelekwa kwenye Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Babati.
MHE. LUCY J. SABU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka CCTV camera na alarm systems katika masoko, shule na sehemu za wazi zenye mkusanyiko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalumu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ili kudhibiti majanga mbalimbali katika taasisi, Serikali imekwishachukua hatua mbalimbali ambapo kupitia Mpango wa Uendelezaji Miji ya Kimkakati Tanzania na Mpango wa Uboreshaji wa Miji jumla ya miji 26 iliyotekeleza miradi ya kimkakati ya ujenzi wa masoko, stendi, na bustani za kupumzikia zimefungiwa vifaa vya utambuzi ikiwemo CCTV camera na alarm system. Aidha, ukarabati wa shule 89 kongwe na chakavu uliofanyika umezingatia miundombinu ya kujikinga na majanga hususani majanga ya moto.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishatoa maelekezo katika Mikoa yote nchini kuzingatia ufungaji wa vifaa vya kutambua na kudhibiti majanga mbalimbali katika taasisi. Ahsante sana.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakarabati Kituo cha Afya Bungu Wilayani Korogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Bungu ni kikongwe, chakavu na kipo kwenye eneo finyu. Serikali imefanya tathmini na kuweka mpango wa kujenga kwa awamu Kituo cha Afya kipya kwa gharama ya shilingi milioni 400.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe katika mwaka wa fedha 2023/2024 itatenga kutoka mapato ya ndani shilingi milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya cha Bungu. Aidha, Halmashauri itaendelea kutenga fedha kila mwaka kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Kituo hicho. Ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU K.n.y. MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya maboresho ya ujenzi na ukarabati Vituo vya Afya Chikobe na Bukoli ili vitoe huduma stahiki kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais- TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Geita kwa mwaka 2023/2024 itatenga kutoka mapato ya ndani shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa Kituo cha Afya cha Bukoli. Aidha katika mwaka huo, Halmashauri ya Wilaya ya Geita itatenga shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati katika Kituo cha Afya Chikobe. Ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatenga fedha za ujenzi wa Vituo vya Afya Kata za Ukata na Litumbandyosi, Halmashauri ya Wilaya Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali ilipeleka Shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi Kituo cha Afya cha Kimkakati katika Kata ya Mkumbi iliyopo Tarafa ya Mkumbi. Kituo hiki cha kimkakati kitahudumia Kata sita (6) za tarafa hiyo ikiwemo Kata ya Ukata. Ujenzi wa Kituo hicho cha Afya upo katika hatua za umaliziaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga katika mwaka 2022/2023, imetenga Shilingi milioni 500 fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Litumbandyosi.
MHE YUSTINA A. RAHHI aliuliza: -

Je, kuna manufaa gani ya kuunganisha Idara ya Kilimo na Mifugo katika Halmashauri za Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekit, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yustina Arcadius Rahhi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchakato wa uandaaji wa muundo na mgawanyo wa majukumu huzingatia mambo mbalimbali ikiwemo Sera, Sheria na maelekezo ya Serikali ya wakati husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muundo na Mgawanyo wa Majukumu ya Halmashauri za Wilaya uliidhinishwa rasmi tarehe 29 Januari, 2022, baada ya kufanya mapitio kwa kushirikisha wadau mbalimbali. Katika mabadiliko hayo, Idara ya Kilimo, Umwagiliaji na Ushirika na Idara ya Mifugo na Uvuvi iliunganishwa na kuwa Idara moja ya Kilimo na Mifugo kutokana na kushabihiana kwa majukumu ya Idara ya Kilimo na Mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, manufaa ya kuhuisha miundo katika ngazi ya halmashauri na Mikoa ni kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa majukumu, kupunguza gharama za uendeshaji na kuimarisha uratibu na usimamizi. Hivyo, muundo mpya wa halmashauri umepungua kutoka Idara 13 na Vitengo Sita na kuwa na Idara Tisa na Vitengo Tisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Muundo na Mgawanyo wa Majukumu wa Taasisi hizo unaweza kufanyiwa mabadiliko inapohitajika bila kuathiri ufanisi ili kukidhi utendaji kazi wa kila siku. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawalipa Watumishi waliohamishiwa katika Halmashauri ya Chemba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ilianzishwa rasmi tarehe Mosi Julai, 2013, baada ya Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa kugawanywa. Jumla ya watumishi 90 wa idara mbalimbali za Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa, walihamishiwa Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ambao walistahili kulipwa kiasi cha Shilingi milioni 238.7 ikiwa ni stahiki zao za kiutumishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba ilihakiki madeni ya watumishi hao na kuwasilisha Serikali Kuu maombi ya kulipwa madeni hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Chemba katika mwaka wa fedha 2023/2024, itatenga shilingi milioni 50 kwa ajili ya kulipa madeni hayo. Aidha, Serikali itaendelea kutenga fedha katika bajeti za kila mwaka ili kuendelea kulipa madeni hayo.
MHE. JACKSON G. KISWAGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za kujenga Vituo vya Afya katika Kata ya Lyamugungwe na Kihanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais,TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jackson Gedion Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilipeleka Shilingi bilioni 1.3 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vitatu katika Wilaya ya Iringa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Iringa kupitia mapato ya ndani imetenga Shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Magulilwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya Kata ya Lyamungungwe na Kihanga, Serikali itajenga Kituo cha Afya cha kimkakati katika Kata ya Kihanga ambayo itatengewa fedha kwenye bajeti ya mwaka 2024/2025. Ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, ni lini Maboma ya Zahanati Vijiji vya Lata, Ikigijo, Lukale, Malwilo, Bulyanaga, Shushuni, Nata, Usiulize na Igushilu yatakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilipeleka Shilingi milioni 200 katika Wilaya ya Meatu kwa ajili ya ukamilishaji wa Zahanati nne. Aidha, katika mwaka 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi milioni 200 kutoka Serikali Kuu na Shilingi milioni 100 kutoka mapato ya ndani ya Halmashauri kwa ajili ya ukamilishaji wa Zahanati za Mwandukisesa, Masanga, Mwanyahina, Mwabagashi na Ikigijo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 kiasi cha Shilingi milioni 100 kitatengwa kutoka mapato ya ndani ya Halmashauri kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati za Igushilu na Nata. Ahsante.
MHE ANTON A. MWANTONA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukarabati majengo ya Zahanati ya Ukoma kuwa Kituo cha Afya cha Kata ya Kisondela Wilayani Rungwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Majengo ya Zahanati ya Makete, Ukoma yaliyokuwa yakitumika kwa wagonjwa wa ukoma ni chakavu. Aidha, kwa kuwa eneo la Kata hii halikidhi vigezo vya kuwa na Kituo cha Afya cha Kimkakati kwa kuzingatia idadi ya watu wasiofikia angalau 10,000, Serikali itaendelea kuitumia zahanati inayotumia moja ya majengo haya kutoa huduma kwa wananchi wa eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kata hiyo itakapokidhi vigezo vya kuwa na Kituo cha Afya cha kimkakati, Serikali itafanya maamuzi stahiki. Ahsante.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU K.n.y. MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za watumishi waliohamishiwa Halmashauri mpya Nzera?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Musukuma Joseph Kasheku Mbunge wa Jimbo la Geita Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitenga kiasi cha Shilingi Milioni 150 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya Mkurugenzi katika Halmashauri ya Wilaya ya Geita, ambapo ujenzi wa nyumba hiyo unaendelea na upo katika hatua ya upauaji.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Geita imetengewa kiasi cha Shilingi Milioni 240 kwa ajili ya ujenzi wa nyumba mbili (2) za Wakuu wa Idara.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Geita na Halmashauri nyingine kote nchini zenye upungufu wa nyumba za watumishi kuendelea kutenga bajeti za mapato ya ndani kila mwaka ili kutatua changamoto za upungufu wa nyumba za watumishi. Ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuboresha Wodi za Wazazi nchini pamoja na kuongeza huduma hizo kwa Wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka 2018/2019 mpaka sasa, Serikali imejenga Hospitali mpya za Halmashauri 127 kati ya hizo Hospitali 70 zimeshasajiliwa na kuanza kutoa huduma kwa wananchi ikiwemo huduma za dharura, upasuaji na wodi za Wazazi.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hicho, Vituo vya Afya 822 vimekarabatiwa na kujengwa ambapo kati ya hivyo 476 vinatoa huduma za dharura, upasuaji na wodi za wazazi. Wodi za Wazazi zimeboreshwa kwa kuweka maeneo yote muhimu kwa huduma za uzazi salama.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 12.5 kwa ajili ya kujenga hospitali 25 zitakazokuwa na Wodi za Wazazi.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya Kata ya Kagera/Nkanda Wilayani Kasulu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 ilipeleka Shilingi Bilioni 1.4 kwenye Halmashauri ya Wilaya Kasulu kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya vya Kitanga, Nyenge na Rungwe Mpya. Ujenzi wa vituo hivi upo hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024 itatenga fedha Shilingi Milioni 500 kutoka kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Kagera/Nkanda.
MHE. TARIMBA G. ABBAS aliuliza: -

Je, kuanzia mwaka 2015 hadi 2020 ni fedha kiasi gani kwa ajili ya vijana, akinamama na watu wenye ulemavu zimekopeshwa na kurejeshwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa mikopo inayotokana na asilimia kumi ya mapato ya ndani ya halmashauri kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamia mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka 2015 hadi mwaka 2020 Serikali kupitia mapato ya ndani ya halmashauri ilitoa mikopo ya jumla ya shilingi bilioni 133. Katika kipindi hicho jumla ya shilingi bilioni 92.21 sawa na asilimia 69.32 zilirejeshwa kutoka kwa vikundi vya wanufaika.
MHE. VENANT D. PROTAS K.n.y. MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza majengo katika Kituo cha Afya Itobo Wilayani Nzega?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaqueline Kainja Andrea, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza kuongeza majengo katika Kituo cha Afya Itobo kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Nzega. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Shilingi milioni 500 zilipelekwa kwa ajili ya ujenzi wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje, jengo la maabara, kichomea taka, jengo la mama na mtoto, jengo la upasuaji na jengo la kufulia nguo. Ujenzi wa majengo haya upo katika hatua mbalimbali za ukamilishaji. Ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kusaidia Hospitali ya Wilaya ya Serengeti na Nyerere DHH kwa kuzijengea uwezo wa kutoa huduma bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kuanzia mwaka wa fedha 2017/2018 mpaka 2021/2022, imepeleka fedha Shilingi bilioni 2.36 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kwa ajili ya kuboresha huduma zinazotolewa kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti. Fedha hizo zimetumika kujenga majengo saba (7) ya kutolea huduma ambapo majengo sita yamekamilika na yanatoa huduma na jengo moja la Wodi ya Mama na Mtoto lipo kwenye hatua ya ukamilishaji. Aidha, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022, imepeleka katika hospitali hiyo watumishi 16 na vifaa na vifaatiba mbalimbali vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, Hospitali Teule ya Nyerere (Nyerere DDH) katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepokea vifaa tiba mbalimbali vya kutolea huduma za afya ikiwemo haematology machine, biochemistry machine na urine analyser. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Hospitali hii imetengewa bajeti ya kuajiri watumishi saba (7) wa kada mbalimbali za afya.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Madiwani wa Halmashauri ya Mji wa Makambako wataongezewa posho kama ilivyo katika Halmashauri nyingine nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga Mbunge wa Jimbo la Makambako kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikiwalipa Madiwani wa Mamlaka za Serikali za Mitaa ikiwemo Halmashauri ya Mji Makambako posho kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura 287 na 288 na kwa kuzingatia Kanuni za Kudumu za Halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwaka 2019 Halmashauri ya Mji Makambako imekuwa ikilipa posho ya vikao ya Shilingi 50,000 ikiwa ni Shilingi 10,000 zaidi ya kiwango kilichopendekezwa. Aidha, hivi sasa viwango vya posho za safari kwa Halmashauri hiyo vinalipwa kwa kuzingatia waraka wa zamani kwa sababu viwango vya posho mpya havikutengewa bajeti ya mwaka 2022/2023, kwa kuwa wakati maelekezo ya mabadiliko ya posho hizo yanatoka tayari Bajeti ya Halmashauri ilikuwa imeandaliwa na kupitishwa kwenye vikao vya Kisheria vya Maamuzi.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mji wa Makambako inashauriwa kufanya mapitio ya bajeti au izingatie maelekezo ya Waraka Na. 1 wa Utumishi wa Umma wenye Kumb. Na. CAC.17/228/01/A/176 wa Tarehe 10 Juni, 2022 kwenye bajeti ya mwaka ujao wa fedha.
MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza: -

Je, Jiji la Arusha lina wamachinga wangapi, wapo maeneo gani na wangapi wamepatiwa vitambulisho hadi kufikia mwezi Februari, 2022?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hadi kufikia mwezi Februari, 2022 Jiji la Arusha lilikuwa na wamachinga 5,426 ambao walikuwa wamepangwa katika maeneo mbalimbali kama ifuatavyo; soko la Samunge, Kiwanja Na. 68 Soko la Kilombero, eneo la Ulezi Mianzini, Machame Luxuary na Kilombero eneo la Daladala.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuratibu usajili na utoaji vitambulisho vya wamachinga, ambapo kwa Halmashauri ya Jiji la Arusha jumla ya wamachinga 1,187 sawa na asilimia 22 wamepatiwa Vitambulisho.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI K.n.y. MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la kubebea Wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/ 2022 Serikali kupitia Mpango wa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatagawiwa kwa Halmashauri zote 184. Kupitia utaratibu huu kila Halmashauri itapatiwa gari moja la kubebea wagonjwa, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ununuzi wa magari ya kubebea Wagonjwa ili kuboresha na kuimarisha hali ya utoaji huduma za afya nchini kote.
MHE. MWANTUMU M. ZODO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafanya ukarabati wa Hopsitali ya Wilaya ya Pangani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshemiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Mzamilu Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 21 kwa ajili ya kufanya ukarabati wa Hospitali kongwe 21 ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Pangani. Aidha, kupitia mpango huo, kila hospitali kongwe imetengewa shilingi bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kukarabati hospitali za Halmashauri ambazo miundombinu yake imechakaa ili kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini kote.
MHE. DANIEL B. SILLO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itasaidia ujenzi wa Wodi ya Mama na Mtoto na chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya Gidas?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Baran Sillo, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilipeleka shilingi bilioni 1.04 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Babati Vijijini kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri, Kituo cha Afya, Nyumba ya Mtumishi na ukamilishaji wa zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uhitaji wa wodi ya mama na mtoto na chumba cha kuhifadhia maiti katika Kituo cha Afya Gidas.

Mheshimiwa Naibu Spika, kituo hiki kimeombewa fedha Hazina na ujenzi utaanza mara fedha zitakapotolewa.
MHE. ANNE K. MALECELA aliuliza: -

Je, Serikali inajua kwamba Zahanati ndogo ya Vunta iliyopo Kata ya Vunta kwenye Tarafa ya Mamba Vunta imewekwa bango la Kituo cha Afya cha Vunta badala ya Zahanati ya Kijiji cha Vunta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Vunta kilichopo Tarafa ya Mamba Vunta ni miongoni mwa Vituo vya Afya sita vya Serikali vinavyotoa huduma kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Same. Kituo hicho kilipandishwa hadhi na kusajiliwa mwezi Januari, 2004 ambapo kilipewa msimbo namba 108286-6 na kinatambulika kitaifa kama Kituo cha Afya na si Zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya ya Same ilitenga Shilingi milioni 20 kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya ukarabati wa jengo la maabara ambapo ukarabati huo upo katika hatua ya ukamilishaji. Aidha, katika Mwaka 2023/2024 Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Same itafanya ukarabati mkubwa wa Kituo cha Afya na kuongeza miundombinu ya huduma za upasuaji.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kujenga chumba cha upasuaji kwa ajili ya Wajawazito katika Kituo cha Afya cha Itaka Wilayani Mbozi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepeleka shilingi milioni 300 kwenye Kituo cha Afya Itaka katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi. Fedha hizo zinatumika kujenga jengo la wazazi, na jengo la upasuaji. Ujenzi wa majengo hayo upo katika hatua ya msingi.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, ni lini Vituo vya Afya vya Rukaragata na Nemba vitapewa vifaa vya upasuaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023, imetenga shilingi bilioni 69.65 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwa ajili ya vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini. Kati ya fedha hizo Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo imetengewa shilingi milioni 250.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imepeleka vifaa vya upasuaji ikiwemo kitanda, taa ya upasuaji na X-ray machine kwa ajili ya Kituo cha Afya Nemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kituo cha Afya Rukaragata hakina jengo la upasuaji, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo katika mwaka wa fedha 2023/2024, itatenga shilingi milioni 50 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa jengo hilo.
MHE. MARTHA F. MARIKI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwaongezea mkopo akina mama wajasiriamali wa Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri za Mkoa wa Katavi zimekuwa zikitoa mikopo ya uwezeshaji kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri kwa kuzingatia sheria na kanuni za utoaji mikopo hiyo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri za Mkoa wa Katavi zilitoa jumla ya mikopo ya Shilingi milioni 980 sawa na asilimia 105 kwa vikundi 124 vyenye jumla ya wanufaika 850. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 halmashauri za mkoa huo zimepanga kutoa mikopo hiyo yenye jumla ya Shilingi bilioni 1.45 sawa na ongezeko la kiasi cha Shilingi milioni 470.

Mheshimiwa Spika, halmashauri zitaendelea kuongeza kiwango cha mikopo kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kulingana na ongezeko la makusanyo ya mapato ya ndani. Ahsante sana.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Madaktari Bingwa na Wataalam wa Vifaa Tiba katika Hospitali ya Malawi ambayo ipo Kata ya Buza Temeke?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kituo cha kutolea huduma za Afya cha Malawi bado hakijapandishwa hadhi kuwa Hospitali. Kwa sasa Kituo hicho kinatambulika kama Kituo cha Afya - Malawi ambacho hakijakidhi vigezo vya hitaji la kupelekewa Madaktari Bingwa kwa kuzingatia mwongozo wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kwa sasa inaendelea na taratibu za kuongeza Vifaa Tiba kwenye Kituo hicho. Aidha, Halmashari inaelekezwa kutenga fedha za mapato ya ndani kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu inayohitajika ili kiendane na hadhi ya Hospitali na kuombewa kupandishwa hadhi.
MHE. MARIAM N. KISANGI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kuongeza na kujenga maeneo ya kusubiri kuona wagonjwa katika Hospitali nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea na ujenzi wa Hospitali mpya kwenye Halmashauri ambazo hazikuwa na hospitali, ambapo mpaka sasa jumla ya hospitali mpya 127 zinaendelea na ujenzi. Aidha, kumekuwa na changamoto ya kukosekana kwa majengo ya Ndugu wa Wagonjwa kusubiria kuona wagonjwa katika hospitali hizo.

Mheshimiwa Spika, ili kutatua changamoto hiyo, Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024 itatenga bajeti ya shilingi bilioni 2.04 kwa ajili ya ujenzi wa sehemu za kusubiria wagonjwa kwenye hospitali 102 ambazo zinakamilisha ujenzi wa wodi za kulaza wagonjwa. Ahsante.
MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya Ngara?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ngara ni miongoni mwa Halmashauri 25 zilizoanza kutekeleza ujezi wa Hospitali kwa awamu ya tatu katika mwaka wa fedha 2021/2022, ambapo ilipokea fedha shilingi milioni 500 na kuanza ujenzi wa Jengo la Wagonjwa wa nje (OPD) na Jengo la Maabara.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ngara katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetengewa fedha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali. Halmashauri hiyo ilipokea fedha hizo mwezi Novemba 2022 kwa maelekezo ya kutumia fedha hiyo kwa ajili ya ujenzi wa jengo la huduma ya mama na mtoto, pamoja na chumba cha upasuaji wa dharura. Kwa sasa Halmashauri ipo kwenye utaratibu wa kutangaza kazi ili kupata kandarasi ya kusimamia ujenzi, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kujenga soko la Tengeru kwa kiwango cha Kimataifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na soko la kisasa kutokana na ongezeko kubwa la shughuli za kiuchumi katika eneo la Tengeru. Kwa sasa eneo hilo lenye ukubwa wa ekari 2.3 linatumika kama gulio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na uhitaji uliopo eneo hilo ni dogo na halikidhi mahitaji ya soko hilo. Hivyo, Halmashauri ya Meru imetenga eneo la Madiira lenye ukubwa wa ekari 15.5 lenye uwezo wa kubeba miundombinu yote ikiwemo miundombinu kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri inatarajia kukamilisha na kuwasilisha andiko la mradi huo wa kimkakati Ofisi ya Rais, TAMISEMI Februari, 2023 kwa ajili ya maombi ya fedha, ahsante.
MHE. JOSEPH A. TADAYO aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kuweka sharti vikundi vya wanawake na vijana kuwa na mtu mwenye ulemavu kwa mikopo ya Halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Anania Tadayo, Mbunge wa Jimbo la Mwanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya Halmashauri hutolewa kwa mujibu wa Sheria za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo kwa Vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu ya mwaka 2019 na Kanuni zake zilizoboreshwa mwaka 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa masharti yaliyowekwa kwenye kanuni hizo, hazizuii mtu mwenye ulemavu kuwa miongoni mwa vikundi vya wanawake au vijana ikiwa amekidhi mahitaji ya sheria na kanuni zake. Aidha, kundi la watu wenye ulemavu limepewa fursa mahususi ili kuwarahisishia kupata mikopo ya asilimia 10, ahsante.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga stendi ya kisasa Ikungi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi ina uhitaji wa stendi ya mabasi yenye ubora itakayowezesha huduma bora za usafiri.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri imekwishalipa fidia ya eneo la ukubwa wa hekari tano kiasi cha shilingi milioni 36 lililopo katika Kijiji cha Muungano Kata ya Unyahati ili kupisha ujenzi wa stendi hiyo.

Mheshimiwa Spika; katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023, Halmashauri imetenga kiasi cha shilingi milioni 110 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi hiyo.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itazigawa upya Halmashauri nchini ili Wananchi wapate huduma kwa urahisi kutokana na jiografia za Halmashauri hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imekuwa ikigawa maeneo mapya ua Utawala zikiwemo Halmashauri kwa lengo la kusogeza huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa, Serikali inaendelea na ujenzi wa miundombinu ya huduma na kiutawala katika mamlaka mpya ambazo hazina miundombinu hiyo muhimu ili kuziwezesha kutoa huduma bora kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa jumla ya majengo ya utawala 109 yenye thamani ya shilingi bilioni 356.8 yanaendelea kujengwa kote nchini, lengo la Serikali kwa sasa ni kukamilisha miundombinu katika mamlaka zilizopo kabla ya kuanzisha mamlaka mpya, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, ni lini Kata za Sirari na Nyamongo zitapandishwa hadhi na kuwa Mamlaka za Miji Midogo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka kufikia mwezi Januari, 2023, nchi yetu ina jumla ya Halmashauri za Miji 21 na Mamlaka za Miji Midogo 71.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa mwongozo wa uanzishaji wa mamlaka za Serikali za Mitaa wa mwaka 2014, utaratibu wa kuomba kuanzisha Mamlaka za Miji Midogo huanza na mikutano ya kujadili. Mikutano hiyo hufanywa katika ngazi ya vijiji, kisha Kamati ya ushauri ya Wilaya (DCC), Kamati ya ushauri ya Mkoa (RCC) na kuwasilishwa Ofisi ya Rais - TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, kusudio la kuanzisha Mamlaka za Miji Midogo katika Kata za Sirari na Nyamongo mchakato wake uliishia kwenye Kamati ya Ushauri ya Wilaya kwa kikao kilichofanyika mwaka wa fedha 2011/2012. Hivyo, Halmashauri inashauriwa kutimiza matakwa ya mwongozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mpango wa Serikali kwa sasa ni kukamilisha kwanza miundombinu kwa mamlaka zilizopo kabla ya kuanzisha mamlaka mpya. Ahsante.
MHE. VITA R. KAWAWA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa Shilingi Milioni 100 kumalizia Kituo cha Afya Mchomoro zilizoahidiwa na Rais wa Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa Mbunge wa Jimbo la Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Mchomoro kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo kimejengwa kwa nguvu za Wananchi, fedha za Halmashauri, Mfuko wa Jimbo, pamoja na wadau. Ujenzi wake ulianza mwaka 2019 na kiasi cha Shilingi Milioni 52.5 zimetumika, kujenga jengo la wagonjwa wa nje ambalo limekamilika na linatoa huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kituo hiki hakina miundombinu muhimu ya kukiwezesha kutoa huduma za ngazi ya kituo cha afya, Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024, itatenga Shilingi Milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu hiyo. Ahsante.
MHE. SAMWELI X. HHAYUMA aliuliza: -

Je, Serikali haioni umuhimu wa kujenga vyumba vya kujifungulia akina Mama kwenye Zahanati za Dirma, Laghanga na Getanus?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Samweli Xaday Hhayuma, Mbunge wa Jimbo la Hanang, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua umuhimu wa vituo vya kutolea huduma za afya kutoa huduma ya kujifungua, zikiwemo zahanati za Dirma, Laghanga na Getanus zilizopo Halmashauri ya Hanang. Katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali kupitia Halmashauri ya Hanang itatenga kiasi cha shilingi milioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa chumba cha kujifungua katika jengo la Zahanati ya Laghanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, upanuzi wa vyumba vya kujifungua katika zahanati za Dirma na Getanus utafanyika katika mwaka wa fedha 2024/2025. Ahsante.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kushughulikia huduma za afya kwa uchunguzi tiba na kujikinga katika Shule za Msingi na Sekondari?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma ya afya kinga na tiba shuleni ni afua muhimu inayotekelezwa na Serikali kuwajengea watoto uelewa wa kujikinga na magonjwa. Huduma hii inahusisha utoaji wa elimu ya afya, utambuzi wa magonjwa katika hatua ya awali pamoja na uratibu wa kupata matibabu kwenye vituo vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Halmashauri imeendelea kuratibu utolewaji wa elimu na huduma za afya kwa watoto walioko shuleni, hususani kwenye magonjwa ya malaria, minyoo, kichocho, saratani ya mlango ya kizazi, afya ya kinywa, meno pamoja na macho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi cha mwaka 2021/2022, Serikali kwa kushirikiana na wadau wa afya iligawa vyandarua 3,104,401 kwenye shule za msingi 7,639 kwa uwiano wa chandarua kimoja kwa kila mtoto. Pia, chanjo ya kuzuia maambukizi ya saratani ya mlango wa kizazi ilitolewa kwa wasichana 623,501 dozi ya kwanza na 472,460 dozi ya pili. Aidha, kila mwaka hufanyika kampeni ya utoaji dawa za minyoo na matone ya vitamini ‘A shuleni, ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka wahudumu wa afya na madaktari kwenye Vituo vya Afya na Hospitali ya Wilaya ya Tanganyika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Uongozi wa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imeendelea kuboresha huduma za afya kote nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2020/2021 na 2021/2022, Serikali imeajiri watumishi wa kada za afya 10,462 na kuwapanga kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa kuzingatia uhitaji.


Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya ajira 7,612 za kada ya afya zilizotolewa na Serikali mwezi Julai, 2022 Halmashauri ya Wilaya ya Tanganyika ilipangiwa watumishi 62 wa kada mbalimbali ikiwemo Wauguzi na Madaktari kwa ajili ya hospitali, vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuajiri watumishi wa Sekta ya Afya na kuwapeleka katika vituo vya huduma kote nchini ikiwemo Halmashauri ya Tanganyika, ahsante.
MHE. MARIAM N. KISANGI K.n.y. MHE. JACKSON G. KISWAGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Maabara kwenye Zahanati zote za Jimbo la Kalenga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jackson Gedion Kiswaga, Mbunge wa Jimbo la Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuboresha miundombinu ya afya kwa kujenga na kukarabati vituo vya kutolea huduma za afya katika ngazi ya afya ya msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali ilipeleka fedha shilingi bilioni 27.8 kukamilisha maboma ya zahanati 555. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga shilingi bilioni 15 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa maboma ya zahanati 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Kalenga lina jumla ya zahanati 36 na kati ya hizo, zahanati 11 zinatoa huduma za maabara na zahanati 25 zinatoa huduma za maabara za msingi. Ili kuboresha huduma, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya kutolea huduma za maabara katika zahanati zote nchini zikiwepo zahanati za Jimbo la Kalenga, ahsante.
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi ili kuondoa migogoro ya Wakulima na Wafugaji katika Wilaya ya Kilwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane Mbunge wa Jimbo la Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa ina jumla ya vijiji 90 na kati ya vijiji hivi, vijiji 56 vina Mpango wa Matumizi Bora ya Ardhi mpaka kufikia mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa na kumaliza kabisa migogoro ya wakulima na wafugaji ambayo imekuwa ikijitokeza mara kwa mara, Serikali imejipanga kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji sita kwa kila mwaka. Aidha, kwa mwaka huu wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 60 kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji vitatu vya Nandete, Kiranjeranje na Ruhatwe na kufanya urejeaji wa mipango ya matumizi ya ardhi iliyokwisha muda wake katika Vijiji vya Kandawale, Likawage na Nanjilinji B.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na changamoto hizo, halmashauri zote za wilaya nchini zimeelekezwa kutenga fedha kila mwaka katika bajeti zao kwa ajili ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi kwenye maeneo yote ya vijiji ikiwa ni pamoja na kuweka alama zinazoonekana kwa urahisi ili kuwezesha maeneo hayo kulindwa na kuzuia mwingiliano wa kimatumizi unaofanywa na wananchi. Hatua hii itawezesha kumaliza migogoro ya ardhi inayohusisha wakulima na wafugaji, ahsante.
MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa tiba katika Hospitali ya Wilaya ya Mbarali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais -TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita imefanya maboresho makubwa ya miundombinu katika sekta ya afya ikiwemo ujenzi wa hospitali za halmashauri, vituo vya afya na zahanati.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imepeleka vifaa na vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 418 kwa ajili ya jengo la huduma za dharura (EMD), pamoja na mashine ya kisasa ya X-ray ya shilingi milioni 155 hospitali ya Wilaya ya Mbarali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 69.95 katika bajeti ya mwaka 2022/2023 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa na vifaa tiba kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Mbarali ambayo imetengewa shilingi milioni 100, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA K.n.y. MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali ya Wilaya katika Halmashauri ya Wilaya ya Meatu kwa kuwa hospitali iliyopo ina hadhi ya kituo cha afya na haikidhi mahitaji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Meatu ilianza kutoa huduma kwa ngazi ya Kituo cha Afya. Aidha, mwaka 1989 ilipandishwa hadhi na kuwa Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, Hospitali hii ni miongoni mwa hospitali kongwe 50 ambazo katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 16.5 ili kufanya ukarabati wa hospitali 19.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali itatenga fedha za ukarabati wa hospitali 31 zilizobakia ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Meatu, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatambua mipaka ya Halmashauri ya Mkalama na Iramba ili kuondoa migogoro katika Kata za Tumuli, Kinyangiri na Gumanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mgogoro kati ya Kijiji cha Mgungia, Kata ya Maluga, Tarafa ya Kinampanda, Wilaya ya Iramba na Kijiji cha Milade, Kata ya Tumuli, Tarafa ya Kinyangiri Wilaya ya Mkalama ulikuwa ukisababishwa na shughuli za kilimo, ufugaji, pamoja na wananchi kutokuwa na ufahamu wa mipaka yao ya vijiji. Wananchi wa pande zote mbili zenye mgogoro walikubaliana na mipaka iliooneshwa na ndiyo iliyotumika katika zoezi la maandalizi ya Mpango wa Matumizi ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika, mgogoro kati ya Kijiji cha Maluga, Kata ya Maluga, Tarafa ya Kinampanda na Vijiji vya Tumuli na Kitumbili, Kata ya Tumuli, Tarafa ya Kinyangiri ulikuwa ukisababishwa na uwepo wa makosa katika ramani za upimaji wa vijiji ya mwaka 2010. Wataalam wamekutana uwandani na kufanikiwa kuonesha mpaka wa kila kijiji kwa mujibu wa Tangazo la Serikali Namba 446 la mwaka 2013 la uanzishwaji wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, mgogoro wa mpaka kati ya Wilaya ya Iramba, Kijiji cha Kisana, Kata ya Kisiriri na Wilaya ya Mkalama Vijiji vya Kinamkamba na Mghimba, Kata ya Gumanga unasababishwa na wananchi wa pande zote mbili kutotambua mipaka yao. Wataalamu wa ardhi na viongozi kutoka Wilaya zote mbili walifika uwandani mnamo tarehe 19 Januari, 2018 na kufanya zoezi la kuhakiki mpaka pamoja na kutoa eimu kwa wananchi juu ya haki ya umiliki wa ardhi na kutii sheria na taratibu zilizowekwa ili kuepusha migogoro, ahsante sana.
MHE. MUSSA R. SIMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali ya Wilaya Singida Mjini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Ramadhani Sima Mbunge wa Singida Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa fedha Shilingi Bilioni 3.5 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Singida ambapo itakapokamilika Hospitali inayotumika sasa itabaki kuwa Hospitali ya Manispaa.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetenga Shilingi Milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali mpya katika Manispaa ya Singida, ambapo fedha hiyo sasa itatumika kukarabati majengo katika Hospitali ya Mkoa ya sasa ambayo itabadilishwa hadhi kuwa Hospitali ya Manispaa ya Singida. Ahsante.
MHE. FLORENCE G. SAMIZI K.n.y. MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza tatizo la ukosefu wa Watumishi wa Kada mbalimbali katika Hospitali nchini pamoja na ukosefu wa Vifaa tiba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2020/2021 iliajiri Watumishi wa kada za afya 2,726 ambao walipelekwa kwenye vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali inatarajia kuajiri watumishi 7,612 wa kada mbalimbali za afya ambao watapelekwa kwenye Halmashauri zote nchini.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais - TAMISEMI imetenga Shilingi Bilioni 69.95 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba kwa Zahanati, Vituo vya Afya na Hospitali za Halmashauri zilizokamilika.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka Watumishi wa Afya wa kutosha katika Kituo cha Afya cha Itaka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi,Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuajiri na kuwapeleka watumishi katika vituo vya kutolea huduma za afya kote nchini ambapo katika ajira za mwaka 2020/2021 Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi ilipelekewa watumishi 17 na kati yao watumishi Wawili walipelekwa Kituo cha Afya Itaka.

Mheshimiwa Spika, katika ajira za watumishi wa kada za afya 7,612 zilizotangazwa wiki hii, Kituo cha Afya Itaka kitapewa kipaumbele. Ahsante.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaiongezea TARURA fedha ili iweze kuzihudumia barabara za Wilaya ya Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikira Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kyerwa ni Wilaya ambayo kwa jiografia ina milima, miteremko pamoja baadhi ya barabara kupita katika maeneo yenye ardhi oevu. Serikali imekuwa ikitenga fedha kila mwaka kwa ajili ya matengenezo ya barabara na madaraja.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeongeza bajeti ya kuboresha miundombinu ya barabara katika Wilaya ya Kyerwa kutoka Shilingi bilioni 1.39 katika mwaka wa fedha 2020/2021 hadi Shilingi bilioni 2.89. Ongezeko hili linatokana na Serikali kuongeza vyanzo vingine ambavyo ni tozo ya mafuta Shilingi bilioni 1.00, Mfuko Mkuu wa Serikali Shilingi milioni 500.00 na Mfuko wa Barabara Shilingi bilioni 1.39.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuongeza wigo wa matengenezo ya barabara pamoja na kufungua barabara mpya katika Wilaya ya Kyerwa kadri ya upatikanaji wa fedha. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itarudisha hekta elfu nane zilizopo kwenye Pori la Ruande Jimbo la Geita kwani pori hilo limepoteza sifa ya kuwa Hifadhi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Kasheku Musukuma, Mbunge wa Geita Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Msitu wa Hifadhi Ruande ulianzishwa kwa GN Na.106 ya mwaka 1956 una ukubwa wa Hekta 15,550. Msitu huu unaosimamiwa na Halmashauri ya Wilaya ya Geita umekuwa ukivamiwa kwa shughuli za kilimo na ufugaji unaofanywa na wananchi wa vijiji 13 vinavyouzunguka.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilipokea maombi kutoka katika Vijiji viwili (2) vya Kagu na Kakubilo ya kumegewa sehemu ya hifadhi hiyo kwa shughuli za kilimo. Serikali inayafanyia tathmini maombi hayo kupitia Kamati ya Mawaziri Nane wa Kisekta inayoshughulikia migogoro ya vijiji 975 nchini kote na itatoa maamuzi muafaka kwa kuzingatia maslahi ya pande zote.
MHE. ISSA J. MTEMVU aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa Kituo Kikuu cha Mabasi cha Magufuli utakamilika pamoja na kuhakikisha Kituo hiki kinafanya kazi kama kilivyokusudiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Jimbo la Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Mabasi cha Magufuli kinachoendelea na ujenzi katika eneo la Mbezi Luis kilianza ujenzi Januari, 2019 kwa mkataba wa miezi 18, hivyo ujenzi ulipaswa kukamilika Julai, 2020.

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi aliongezewa muda wa ujenzi hadi Juni, 2022 kutokana na kuchelewa kutolewa kwa msamaha wa kodi wa vifaa vya ukamilishaji wa ujenzi huo.

Mheshimiwa Spika, hadi mwezi Machi, 2022, kiasi cha shilingi bilioni 53.09 sawa na asilimia 94.73 zilikuwa zimelipwa kukamilisha ujenzi. Aidha, tarehe 14 Machi, 2022, Serikali imetoa msamaha wa kodi na sasa Mkandarasi anaendelea na manunuzi ya vifaa ili kazi ya ujenzi iendelee na kukamilika ifikapo mwezi Juni, 2022. Kukamilika kwa kazi hizo kutafanya kituo hicho kutoa huduma kwa wananchi kama ilivyokusudiwa.
MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Vifaa Tiba katika Hospitali ya Ilongero pamoja na Vituo vya Afya vya Msange na Mgori Wilayani Singida?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ramadhani Ighondo, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali ilipeleka Bohari Kuu ya Dawa Shilingi Bilioni 34 kwa ajili ya ununuzi wa Vifaa Tiba. Tayari Vifaa Tiba vimeanza kusambazwa kwenye Hospitali 67 za Halmashauri ikiwa ni pamoja na Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida ambayo imekwishapokea vifaa vya aina 17 vikijumuisha vifaa vya upasuaji na maabara.

Mheshishimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/ 2023 Serikali imetenga Shilingi bilioni 69.95 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba vitakavyopelekwa kwenye hospitali, vituo vya afya na zahanati zilizokamilika.
MHE. ATHUMANI A. MAIGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itabadilisha mtambo wa kutengeneza hewa ya Naitrojeni Kituo cha Afya Upuge na kuleta mtambo wa hewa ya Oksijeni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Athumani Almas Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Upuge kilifungiwa mtambo wa kutengeneza vacuum mwaka 2012 kwa ajili ya huduma za dharura na upasuaji. Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imefanya tathmini ya mitambo hiyo na matengenezo madogo ya kuzibua njia ya hewa yatafanyika ili iweze kutumika.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepanga kununua mitambo 10 ya kuzalisha hewa ya Oksijeni . Mitambo hiyo itazalisha hewa na kusambaza kwenye vituo vya kutolea huduma za afya ikiwemo Kituo cha Afya cha Upuge ambacho kimefungiwa mfumo wa kupokea na kutawanya hewa ya Oksijeni. Ahsante.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA K.n.y. MHE. ALLY Y. MHATA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka magari ya kubebea wagonjwa katika Vituo vitatu vya Afya Wilayani Nanyumbu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Yahaya Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Nanyumbu ina magari mawili ya kubebea wagonjwa ambayo yanatumika katika Hospitali na Vituo vya Afya. Hata hivyo, magari haya bado ni machache kwa kuzingatia uhitaji uliopo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ambapo kila Halmashauri itapata gari la kubebea wagonjwa ikiwemo Halmashauri ya Nanyumbu. Ununuzi huu utaboresha huduma za afya za dharura na rufaa. Ahsante.
MHE. RASHID A. SHANGAZI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaugawa Mkoa wa Tanga ili kuongeza ufanisi katika eneo la Utawala Bora?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi Mbunge wa Jimbo la Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuanzisha Mkoa, Wilaya na Tarafa mpya umebainishwa kupitia Sheria ya Uanzishwaji wa Mikoa na Wilaya Sura ya 397 (The Regions and Districts Establishment Procedure) Act, 2020) na Mwongozo wa vigezo vya Maeneo Mapya ya Utawala wa mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hii, hatua ya awali inahusisha kupata ridhaa ya Vijiji, Kamati za Maendeleo za Kata, Mabaraza ya Madiwani ya Halmashauri zilizomo katika Mkoa, Kamati za Ushauri za Wilaya, na Kamati ya Ushauri ya Mkoa Mama. Baada ya hatua hiyo, maombi hayo yanawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na tathmini na baadaye kuwasilishwa kwa Mamlaka husika kwa maamuzi kadri itakavyoona inafaa.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI, haijapokea wasilisho la mapendekezo ya kugawa Mkoa wa Tanga. Hivyo, nashauri taratibu za uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala zifuatwe. Ahsante.
MHE. VENANT D. PROTAS aliuliza: -

Je lini Serikali itaigawa Halmashauri ya Wilaya Uyui, ili itoe Halmashauri nyingine ya Igalula kwa kuwa inakidhi vigezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daud Protas Venant, Mbunge wa Jimbo la Igalula kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, halmashauri huanzishwa kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura ya 287 na 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa Mwaka 2014. Mwongozo huo umeainisha vigezo na taratibu zinazopaswa kufuatwa ili kuanzisha halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hii, hatua ya awali inahusisha kupata ridhaa ya vijiji, Kamati za Maendeleo za Kata, Baraza la Madiwani la Halmashauri, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC). Baada ya hatua hii, maombi hayo yanawasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI kwa ajili ya uhakiki na tathmini na kuwasilishwa kwa Mamlaka husika ili itoe uamuzi.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI haijapokea maombi ya kuigawa Halmashauri ya Uyui. Hivyo, nashauri taratibu za uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala zifuatwe. Ahsante.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza watumishi katika Manispaa ya Mpanda hasa katika maeneo ya afya, elimu na maendeleo ya jamii?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Mpanda ina jumla ya watumishi 1,226 kati ya watumishi 1,773 wanaohitajika sawa na asilimia 69.1.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuajiri watumishi kwa awamu ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 watumishi 7,612 wa kada za afya na watumishi 9,800 wa kada za elimu wataajiriwa. Ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA K.n.y. MHE. MARIAM M. NYOKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Hospitali ya Wilaya ya Songea?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mariamu Madalu Nyoka Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kati ya mwaka wa fedha 2019/2020 hadi 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya ya Songea imepokea Shilingi bilioni 3.1 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Jumla ya majengo 14 yamejengwa kwenye Hospitali hiyo ambapo majengo saba yamekamilika na majengo mengine saba ujenzi wake unaendelea katika hatua mbalimbali za ukamilishaji. Ahsante.
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA K.n.y. MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kugawa Mkoa wa Tabora na kupata Mkoa wa Manonga ili kurahisisha shughuli za kiutawala na kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuanzisha Mkoa, Wilaya na Tarafa mpya umebainishwa kupitia Sheria ya Uanzishwaji wa Mikoa na Wilaya na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa mwaka 2014.

Mheshimwa Spika, kwa mujibu wa Sheria hii maombi ya kuanzishwa Mkoa mpya hupata ridhaa ya vijiji, kamati za maendeleo za kata, mabaraza ya Madiwani ya halmashauri zilizomo katika mkoa, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) ya Mkoa Mama.

Mheshimiwa Spika, katika Kikao cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) cha tarehe 3 Machi, 2022 yaliwasilishwa mapendekezo ya kugawa Mkoa wa Tabora, ambapo ilipendekezwa suala hilo kuwasilishwa katika kikao Maalum cha Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kitakachofanyika Mei, 2022.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais TAMISEMI itakapopokea mapendekezo hayo, itafanya uhakiki na tathmini kisha itawayasilisha katika Mamlaka husika kwa ajili ya maamuzi kadiri itakavyoona inafaa.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari ya wagojwa katika Wilaya ya Kilindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua Mbunge wa Kilindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Kilindi ina gari mmoja la kubebea wagonjwa lililopo kwenye Kituo cha Afya Songe ambalo hutumika kubeba Wagonjwa kwenye Vituo vya Kutolea Huduma za Afya. Uwepo wa gari hilo hautoshelezi kukidhi mahitaji ya halmashauri hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO 19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambapo kila Halmashauri itapata gari moja, ikiwemo Halmahsauri ya Kilindi. Ununuzi wa magari haya utaboresha hali ya utoaji huduma za afya kote nchini. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itarejesha fedha Shilingi milioni 204 iliyorudishwa Mwaka wa Fedha 2019/2020 ili iweze kukamilisha ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Biharamulo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais-TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eng. Ezra John Chiwelesa Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Sheria ya Bajeti Na. 11 ya Mwaka 2015 na kanuni zake iliweka utaratibu kwa halmashauri zote nchi, kuomba kibali Wizara ya Fedha na Mipango kwa fedha za miradi zinazotarajiwa kuvuka mwaka wa fedha husika kurejeshwa mfuko mkuu wa Serikali. Maombi hayo yalipaswa kufanyika siku 15 kabla ya tarehe 30 Juni ya mwaka husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo haikufuata utaratibu huo. Hivyo, hali hiyo ilisababisha fedha hizo kurejeshwa katika mfuko mkuu wa Serikali. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilipeleka shilingi milioni 300 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali hiyo, na katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga shilingi milioni 750 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali hiyo. Ahsante.
MHE. NOAH L. SAPUTU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Jengo la Wagonjwa wa Nje, Jengo X-Ray, Jengo la Watoto na Jengo la Utawala katika Hospitali ya Wilaya Olturumet Halmashauri ya Arusha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mbunge wa Jimbo la Arumeru Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Rais- TAMISEMI mwezi Aprili, 2021 ilipokea maombi maalum ya shilingi milioni 800 kwa ajili ya upanuzi na ukarabati wa Hospitali ya Olturumet ambayo miundombinu yake imechakaa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni 16.55 kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali Kongwe 19 nchini. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa awamu kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa Hospitali Kongwe nchini ambapo Hospitali ya Olturumet itapewa kipaumbele.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa mafunzo kwa makundi ya vijana na wanawake wanaopata mikopo ili waweze kujiwezesha kiuchumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma Mbunge wa Jimbo la Bububu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni ya 23 ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu Wenye Ulemavu pamoja na marekebisho yake, Mamlaka za Serikali za Mitaa zimeelekezwa kutenga fedha kutoka katika fedha za marejesho ya mikopo hiyo kwa ajili ya kuwajengea uwezo pamoja na ufuatiliaji wa shughuli za vikundi kwa vikundi vilivyokubaliwa kupata mikopo.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya vikundi 6,317 vya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu katika halmashauri zote nchini vimepatiwa mafunzo kuhusu masuala ya uongozi, usimamizi wa fedha, uendeshaji wa miradi na utoaji wa taarifa.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaajiri watumishi 40,000 katika Mamlaka za Serikali za Mitaa kama ilivyopitishwa katika Bajeti wa mwaka 2021/2022?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia Paulo Issaay Mbunge wa Jimbo la Mbulu Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 tayari Serikali imekwishatoa Ikama na Kibali cha ajira kwa halmashauri zote nchini ambapo jumla ya nafasi za ajira za watumishi 17,412 wa kada ya afya na elimu zimetangazwa. Taratibu za kuajiri watumishi hao zinaendelea kukamilishwa. Aidha, ajira za kada zingine zinaendelea kutolewa kupitia Sekretarieti ya Ajira katika Utumishi wa Umma na halmashauri husika, ahsante.
MHE. ESTHER N. MATIKO K.n.y. MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni vigezo gani vinapaswa vifuatwe na halmashauri ili fedha za maendeleo ziweze kutolewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, utoaji wa fedha za maendeleo zilizotengwa katika bajeti hutolewa kwa halmashauri kwa kuzingatia Waraka na Mwongozo wa Wizara ya Fedha na Mipango kila mwaka kwa kuzingatia maelekezo ya Kifungu Na. 5 cha Kanuni za Sheria ya Bajeti Sura 439, Kifungu cha 6 cha Sheria ya Fedha za Umma, Sura 348 na Kifungu cha 12 cha Sheria ya Bajeti Sura 439.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya vigezo hivyo ni pamoja na halmashauri kuwasilisha maombi ya fedha za utekelezaji ikionesha utayari wa kuanza kutekeleza mradi mara baada ya kupokea fedha. Ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA aliuliza: -

Je ni lini Kituo cha Afya Mapera kilichopo Mbinga Vijijini Kitaanza kutoa huduma za Mionzi na Ultra sound?
NAIBU WAZIRI , OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya cha Mapera kilipokea fedha Shilingi Milioni 400 mwaka wa fedha 2019/ 2020 kwa ajili ya ukarabati mkubwa na upanuzi wa Kituo. Kituo hicho kimekamilika na kuanza kutoa huduma za upasuaji toka Julai 2021 na jumla ya Wakinamama 114 wamekwisha pata huduma ya upasuaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Wananchi wa Kata ya Mapera wanapata huduma ya X- Ray kwenye Kituo cha Afya cha Maguu kilichopo kilometa tatu kutoka kwenye Kituo cha Afya Mapera. Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga inashauriwa kutenga fedha kutoka kwenye mapato ya ndani kwa ajili ya kujenga jengo la X-ray ili Serikali ikipatie Kituo hicho mashine ya X-ray. Ahsante.
MHE. ELIBARIKI E. KINGU K.n.y MHE. JERRY W. SILAA aliuliza: -

Je, Serikali haioni ni wakati muafaka sasa kuwaingiza Wazee na Wanaume kwenye mikopo inayotolewa na Serikali kupitia Halmashauri kwa kuwa kwa sasa wameachwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry William Silaa Mbunge wa Jimbo la Ukonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa sheria ya mikopo ya asilimia 10 na kanuni zake, mikopo hii inatolewa kwa ajili ya kuwezesha makundi maalum ya wanawake, vijana na watu wenye ulemavu kupata mikopo yenye masharti nafuu. Makundi haya kwa kiasi kukubwa hayawezi kupata mikopo katika taasisi nyingine za fedha kwa sababu ya kukosa dhamana na uwezo mdogo wa kumudu riba ili waweze kushiriki katika shughuli za kiuchumi na kujiongezea kipato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kufanya tathmini ya utoaji na urejeshaji wa mikopo hii tangu kutungwa kwa sheria. Tathimini hii itawezesha kushauri namna bora ya utoaji wa mikopo pamoja na mapitio ya Sheria. Ahsante.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha ujenzi wa Vituo vya Afya vya Rugaragata, Kalenge na Nyabuozi – Biharamulo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vituo vya afya vya Rugaragata, Kalenge na Nyabuozi ni miongoni mwa vituo vya muda mrefu na miundombinu yake inahitaji maboresho kulingana na mahitaji ya sasa.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 Serikali itatenga bajeti ya shilingi bilioni 8.75 kwa ajili ya ujenzi, upanuzi na ukamilishaji wa vituo vya afya 20 katika Halmashauri, ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Biharamuro iliyotengewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya upanuzi wa vituo vya afya viwili kati ya vitatu vyenye mahitaji.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa vituo vya afya chakavu ni endelevu. Ahsante.
MHE. SHALLY J. RAYMOND K.n.y. MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta Sheria Bungeni kuruhusu Halmashauri kuzikopesha SACCOS za vijana na wanawake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mikopo ya asilimia 10 inatolewa kwa mujibu wa kifungu cha 37A cha Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura ya 290. Kifungu hicho kimeeleza kwamba Halmashauri zote zinapaswa kutenga asilimia 10 ya mapato yake ya ndani kwa ajili ya mikopo isiyo na riba kwa vikundi vilivyosajiliwa vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu.

Mheshimiwa Spika, mikopo ya SACCOS huendeshwa kwa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha (Vyama vya Ushirika wa Akiba na Mikopo) ya mwaka 2019 ambapo mikopo hiyo hutolewa kwa wanachama wa SACCOS kwa riba. Hivyo, mapendekezo ya kurekebisha Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa Sura ya 290 ili kuzikopesha SACCOS kutaondoa kusudio la kutoa mikopo isiyo na riba kwa wanawake, vijana na watu wenye ulemavu.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza: -

Je, nini mpango wa Serikali kumaliza ujenzi wa zahanati kwa vijiji vilivyokamilisha ujenzi wa maboma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba wa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi ambapo katika kipindi cha mwaka wa fedha wa 2017/2018 hadi 2021/2022 kiasi cha shilingi bilioni 71.95 zimetolewa kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma 1,214 ya zahanati nchini kote. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 15 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati 300, hadi kufikia Februari, 2023 kiasi cha shilingi bilioni 14.6 zimekwishatolewa.

Mheshimiwa Spika, Jumla ya zahanati 762 kati ya 1,514 ujenzi umekamilika na zimeanza kutoa huduma. Aidha, Ujenzi wa maboma 752 ya zahanati upo katika hatua mbalimbali za ukamilishaji.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya zahanati yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi.
MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza: -

Je, ni lini mfumo wa utawala wa Serikali za Mitaa utaanza kufanya kazi katika Kambi za Wakimbizi Mishamo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Makazi ya Wakimbizi ya Mishamo yaliyopo Mkoa wa Katavi, Wilaya ya Tanganyika yalisajiliwa rasmi mwaka 1979. Baada ya usajili, Shirika la Dini la Tanganyika Christian Refugee Services lilipewa jukumu la kusimamia Makazi hayo na kutoa huduma za kijamii ikiwa ni pamoja na kufanya mpango wa kugawanya mitaa. Kupitia Mpango huo ilipatikana mitaa 21 iliyotambuliwa kwa namba kutoka mtaa namba 1 hadi 21.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa mitaa hiyo inatambulika kama vijiji baada ya wakazi hao kutumia majina badala ya namba zilizosajiliwa awali. Aidha, kuanzia Mwaka 1980 Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la UNHCR imekuwa ikitoa huduma za kijamii ikiwemo ujenzi wa shule, zahanati na barabara katika Makazi ya Wakimbizi Mishamo.

Mheshimiwa Spika, Maeneo haya yanaendelea kutambulika kupitia Gazeti la Serikali namba 537 la tarehe 19/07/2019. Aidha, Maeneo hayo bado yapo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na mara yatakapokabidhiwa Ofisi ya Rais TAMISEMI mfumo wa Utawala wa Serikali za Mitaa utaanza kufanya kazi.
MHE. ATHUMAN A. MAIGE aliuliza: -

Je, ni lini Barabara ya Manoleo hadi Kituo cha Afya Upuge itajengwa kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Athuman Almas Maige, Mbunge wa Jimbo la Tabora Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Manoleo - Kituo cha Afya Upuge yenye urefu wa kilometa 22.10 imesajiliwa kwa jina la Nyambele – Upuge – Muhogwe - Magiri ambapo kutokana na umuhimu wake imeendelea kutunzwa kwa kuwekewa kipaumbele kwenye bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa barabara hii, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha changarawe kilometa 13 na kujenga makalavati saba, ambapo ipo hatua ya uandaaji wa nyaraka za zabuni kwa ajili ya kumpata Mkandarasi. Ujenzi unatarajiwa kuanza mwezi Mei, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutafuta fedha ili Barabara ya Nyambele – Upuge – Muhogwe – Magiri yenye urefu wa kilometa 22.10 iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Aidha, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali itatenga shilingi milioni 91.8 kwa ajili ya matengenezo ya kawaida kilometa 15, ujenzi kwa kiwango cha changarawe kilomita mbili na kunyanyua tuta na kujenga makalvati mawili, ahsante.
MHE. HASSAN S. MTENGA aliuliza: -

Je, ni lini jengo la Manispaa ya Mtwara Mikindani litajengwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Seleman Mtenga, Mbunge wa Jimbo la Mtwara Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jengo la Utawala la Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara – Mikindani lilijengwa mwaka 1948. Hivyo, jengo hilo limechakaa na halitoshelezi mahitaji ya Ofisi. Serikali inatambua umuhimu wa Halmashauri hiyo kujengewa jengo jipya kwa matumizi ya Ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwezi Novemba, 2022 Halmashauri iliwasilisha maombi ya kutengewa bajeti katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la utawala na nyumba ya Mkurugenzi. Serikali itatenga bajeti ya shilingi milioni 180 katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya ujenzi wa Nyumba ya Mkurugenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele cha kukamilisha majengo ya utawala yaliyoanza kujengwa kisha itaendelea na ujenzi wa majengo mapya ya utawala likiwemo jengo la Halmashauri ya Mtwara Mikindani. Ahsante.
MHE. LUCY J. SABU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya ukarabati wa miundombinu ya Hospitali ya Mji wa Bariadi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy John Sabu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati wa hospitali kongwe nchini. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 17.1 kwa ajili ya ukarabati wa hospitali 19, ikwemo Hospitali ya Mji wa Bariadi. Aidha, hadi kufikia mwezi Februari, 2023 kiasi cha shilingi bilioni 12.95 zimekwishatolewa kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya hospitali kongwe 14 ambapo hospitali ya Mji wa Bariadi imepelekewa shilingi milioni 900 na kazi za ujenzi zinaendelea, ahsante.
MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawaajiri walimu wanaojitolea katika Jimbo la Kiteto?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshiwa Edward Kisau Olelekaita, Mbunge wa Jimbo la Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto ina jumla ya walimu 752 wa shule za msingi na walimu wa kujitolea 86. Aidha, kwa shule za sekondari kuna jumla ya walimu 298 na walimu wa kujitolea 34.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa Walimu wa kujitolea katika shule za msingi na sekondari na kwa kuwa Serikali huajiri kulingana na upatikanaji wa fedha. Hivyo nafasi za ajira zikitangazwa, tunawashauri Walimu hawa wanaojitolea waombe nafasi hizo ili wale wanaokidhi vigezo waweze kuajiriwa kwa kupewa kipaumbele, ahsante.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka watumishi na vifaa tiba katika Kituo cha Afya Majengo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Dadi Chikota, Mbunge wa Jimbo la Nanyamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua changamoto ya uhaba wa Wataalam wa afya katika vituo vya kutolea huduma za afya nchini. Hata hivyo, Serikali imeendelea kutoa vibali vya kuajiri Watumishi wa Kada ya Afya katika Mamlaka za Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2020/2021 na 2021/2022, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI iliajiri Watumishi wa Kada za Afya 10,328 ambapo Halmashauri ya Mji Nanyamba ilipata watumishi 51 wa kada mbalimbali za afya. Aidha, Kituo cha Afya Majengo kilipangiwa watumishi wanne ambao ni Mteknolojia wa Maabara, Tabibu Msaidizi na Wauguzi wawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imepeleka vifaa na vifaa tiba katika Halmashauri ya Mji Nanyamba vyenye thamani ya shilingi milioni 300 kwa ajili ya vituo vya huduma za afya, ahsante.
MHE. FRANCIS I. MTINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga majengo ya kisasa katika Vituo vya Afya vya Kinyangira na Mkalama katika Halmashauri ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI) naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Isack Mtinga, Mbunge wa Jimbo la Iramba Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kujenga na kukarabati vituo vya afya kwenye Kata za kimkakati ili kusogeza huduma za afya karibu na wananchi. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetoa fedha shilingi bilioni 117 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya 234 kwenye Tarafa na Kata za kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vituo vya Afya vya Kinyangiri na Mkalama ni miongoni mwa vituo vinavyoendelea kutoa huduma katika ngazi ya Kituo cha Afya pamoja na changamoto ya upungufu wa miundombinu hususan ya upasuaji wa dharura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa vituo vya afya nchini kote vikiwemo vituo vya afya Kinyangiri na Mkalama. Ahsante.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza kujenga majengo katika Kituo cha Afya Nguruka kilichopandishwa hadhi ya kuwa Hospitali?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Nguruka kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza Mkoani Kigoma kinahudumia wakazi wapatao 135,546. Kituo kinatoa huduma kwa ngazi ya kituo cha afya kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Uvinza imekwisha jenga hospitali mpya ambayo imeanza kutoa huduma.

Mheshimiwa Spika, kituo hiki kina uhitaji wa majengo mbalimbali ya kutolea huduma ikiwa ni pamoja na wodi mbili za kulaza wagonjwa, kliniki ya mama na mtoto, jengo la kuhifadhia maiti na jengo la kufulia.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023 kituo hicho kimetengewa shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu hiyo itakayowezesha kutoa huduma kwa ngazi ya kituo cha afya. Ahsante.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga barabara ya mchepuko kwa kiwango cha lami kutoka Mpemba kupitia Chapwa Mwakakati katika Mji wa Tunduma kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwa sasa Mji wa Tunduma umekuwa ukikumbwa na msongamano mkubwa wa magari kuanzia Mpemba hadi Forodhani (Boarder) hali inayosababisha usumbufu kwa watumiaji wa barabara ya ndani ya Tunduma na wanaokwenda uelekeo wa barabara ya Tunduma - Sumbawanga.

Mheshimiwa Spika, ili kupunguza adha hiyo, Serikali itatenga kiasi cha shilingi bilioni 1.5 katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya Sogea - Transformer yenye urefu wa kilometa 2.0 kwa kiwango cha lami ili iwe njia mbadala kwa watumiaji wa barabara za Mji wa Tunduma.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya barabara ya mchepuko inayoanzia Mpemba – Chapwa - Makambini kadri ya upatikanaji wa fedha ili kuondoa msongamano mkubwa wa magari. Ahsante.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, ni lini chumba cha kuhifadhia maiti katika Hospitali ya Wilaya ya Tarime TC kitaanza kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Kembaki Michael, Mbunge wa Jimbo la Tarime Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Magena kilichopo Halmashauri ya Mji wa Tarime kimekwishakamilisha ujenzi wa Jengo la kuhifadhia maiti. Aidha, Halmashauri inaendelea na taratibu za ununuzi wa jokofu la kuhifadhia maiti baada ya kupokea fedha za ununuzi wa vifaatiba shilingi milioni 150 kutoka Serikali Kuu katika bajeti ya mwaka wa fedha 2022/2023.
MHE. DOROTHY G. KILAVE aliuliza: -

Je, lini Serikali itawalipa fidia wananchi waliohamishwa kupisha maegesho ya malori eneo la Kurasini tangu mwaka 2015?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy George Kilave, Mbunge wa Jimbo la Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa uthamini uliofanyika mwaka 2013 na ulipaji wa fidia kufanyika Mwaka 2015, Mwekezaji katika mradi huo alitoa shilingi bilioni 16.83 kwa Halmashauri ya Manispaa ya Temeke kwa ajili kulipa fidia ambapo wananchi 165 waliofanyiwa uthamini ili kupisha mradi huo wamelipwa fedha zao kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya malipo hayo kukamilika, wananchi 44 kati ya 165 waliolipwa fidia hawakuridhika na malipo yaliyofanyika, hivyo wakafungua kesi ya madai ya mapunjo ya shilingi bilioni 3.198 katika Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam, kupitia Shauri Namba 50 la mwaka 2016. Tarehe 28 Mei, 2021, Mahakama ilitupilia mbali shauri hilo baada ya wananchi hao kushindwa kuthibitisha madai yao, hivyo, hakuna fidia inayodaiwa na maeneo yaliyotwaliwa kupisha ujenzi wa maegesho ya malori katika eneo la Kurasini kwani wananchi wote wamelipwa kwa mujibu wa sheria, ahsante.
MHE. ANTON A. MWANTONA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa soko la Kimataifa la Ndizi katika Kata ya Kiwira utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwa na Soko la Kisasa la Ndizi, Kiwira, katika Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe. Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe imeanza maandalizi ya kutekeleza mradi huo kwa kufanya Upembuzi yakinifu, kuandaa michoro ya kihandisi, kupima udongo wa eneo la ujenzi na kuandaa andiko la kuomba fedha kwa ajili ya mradi huo.

Mheshimiwa Spika, andiko limewasilishwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa uchambuzi na pindi litakapopitishwa, mradi utatengewa fedha za ujenzi kupitia utaratibu wa miradi ya kimkakati. Ahsante.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza: -

Je, ni Wazee wangapi wamepewa Bima ya Wazee na waliobaki ni lini watapewa Bima hizo Wilayani Kakonko?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Jimbo la Buyungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko inatekeleza afua mbalimbali za afya ikiwemo huduma za afya kwa wazee, kwa kuwapatia vitambulisho vya matibabu bila malipo wazee wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo, kama ilivyo katika Sera ya Wazee ya mwaka 2003, Sera ya Afya ya mwaka 2007 na Mwongozo wa uchangiaji wa huduma za afya nchini.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko iliwatambua wazee wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo wapatao 11,524. Kati yao wazee 6,084 walipewa vitambulisho vya matibabu bila malipo, wazee 2,000 walikatiwa bima ya mfuko wa afya ya jamii ulioboreshwa kupitia mapato ya ndani.

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha wa 2023/2024, Serikali kupitia mapato ya ndani itatenga bajeti kwa ajili ya kuwapatia vitambulisho wazee 3,440 waliobaki katika Halmashauri ya Wilaya ya Kakonko.

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kuwakumbusha viongozi wote wa mikoa na halmashauri kutekeleza maelekezo ya kuwapa vitambulisho vya matibabu bila malipo wazee wote wenye umri wa miaka 60 na kuendelea wasio na uwezo. ahsante.
MHE. DEUS C. SANGU aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupanua Kituo cha Afya cha Laela na kuwa katika hadhi ya Hospitali ya Wilaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deus Clement Sangu, Mbunge wa Jimbo la Kwela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Laela kinamilikiwa na Kanisa Katoliki ambapo Mwaka 2004 kiliingia mkataba wa kutoa huduma na Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ili kuhakikisha wananchi wa Kata ya Laela wanapata huduma za afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali itatenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kipya katika Kata ya Laela ambacho kitakuwa na uwezo wa kutoa huduma za afya pamoja na huduma za upasuaji za dharura.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga imeshajenga Hospitali ya Wilaya, Kituo cha Afya cha Laela kitatoa huduma kwa ngazi ya kituo cha afya, ahsante.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa maboma ya Ofisi Kata za Nkoma, Mwangudo, Mwamanimba na Imalaseko – Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua uwepo wa maboma manne ya Ofisi za Kata ya Nkoma, Mwangudo, Mwamanimba na Imalaseko katika Jimbo la Meatu ambayo yanahitaji kukamilishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Bajeti ya mwaka wa Fedha wa 2023/2024, Halmashauri ya Meatu imetenga fedha za mapato ya ndani kiasi cha shilingi milioni 60 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya Ofisi za Kata ya Imalaseko na Lingeka.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwenye vyanzo mbalimbali kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya ofisi za Kata nchini kote zikiwemo Kata za Nkoma, Mwangudo na Mwamanimba, ahsante.
MHE. ABEID R. IGHONDO K.n.y MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatenga fedha kujenga soko la kisasa Ikungi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Jimbo la Singida Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi imeweka mpango wa kujenga soko la kisasa katika Kijiji cha Ikungi lenye ukubwa wa ekari mbili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa halmashauri inaendelea kufanya mazungumuzo na wananchi ambao wamejenga vibanda vya biashara katika eneo hilo lililoainishwa na mipango miji kwa ujenzi wa soko la kisasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi kwa kushirikiana na UN WOMEN imekamilisha ujenzi wa jengo la mabucha na mbogamboga lenye thamani ya shilingi milioni 82 katika eneo hilo. Aidha, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa soko la kisasa Ikungi, ahsante.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia Watu Wenye Ulemavu mitaji katika Jimbo la Mbogwe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga, Mbunge wa Jimbo la Mbogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2022/2023, Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe ilitenga shilingi milioni 56 kwa ajili ya mikopo ya watu wenye ulemavu. Hadi kufikia mwezi marchi, 2023 jumla ya vikundi 6 vya watu wenye ulemavu vimekopeshwa kiasi cha shilingi milioni 34. Fedha hizi zimewezesha vikundi vya watu wenye ulemavu kuanzisha biashara na kujiongezea kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Halmashauri ya Wilaya ya Mbogwe imetenga shilingi milioni 56.19 kwa ajili ya mikopo isio na riba kwa vikundi vya watu wenye ulemavu. Fedha hizi zitatolewa kupitia mfumo ulioboreshwa wa asilimia 10, ahsante.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka magari ya kubebea wagonjwa katika Vituo vya Afya vya Mtwango na Mgololo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa David Mwakiposa Kihenzile, Mbunge wa Jimbo la Mufindi Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua umuhimu na uhitaji wa magari ya kubebea wagonjwa katika vituo vya kutolea huduma za afya. Kwa kutambua mahitaji yaliyopo, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi bilioni 35.1 kwa ajili ya ununuzi wa magari 316 ya kubebea wagonjwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, taratibu za manunuzi zinaendelea na magari hayo yatagawiwa kwenye halmashauri zote 184 ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ambayo itapewa magari 2 ya kubebea wagonjwa, ahsante.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kukarabati miundombinu ya Hospitali ya Wilaya ya Arumeru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Jimbo la Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali Kongwe Nchini. Katika mwaka wa fedha wa 2022/2023, Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 17.1 kwa ajili ya ukarabati wa hospitali 19. Aidha, hadi kufikia mwezi Februari, 2023, kiasi cha shilingi bilioni 12.95 zimekwishatolewa kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa miundombinu ya hospitali kongwe kumi na nne 14.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali itatenga shilingi bilioni 27.9 kwa ajili ya ukarabati wa hospitali kongwe 31 ikiwepo Hospitali ya Halmashauri ya Meru ambayo imetengewa shilingi milioni 900. Ahsante.
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza: -

Je, ni lini Kituo cha Afya Bukene kitapatiwa mashine ya x- ray na ultrasound?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seleman Jumanne Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Bukene kinatoa huduma za kiuchunguzi ambapo kwa sasa kina mashine ya Ultrasound. Aidha, kituo hiki hakina miundombinu ya jengo la kuwezesha utolewaji wa huduma za X-Ray. Serikali itaendela kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya afya pamoja na ununuzi wa mashine za uchunguzi ikiwemo X-Ray na Ultrasound kwa ajili ya vituo vya huduma nchini ikiwemo Kituo cha Afya cha Bukene, ahsante.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza: -

Je, lini Wananchi wa Busanda watapatiwa Wilaya ya Busanda kama ilivyopendekezwa na Baraza la Madiwani, DCC na RCC Geita?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tumaini Bryceson Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnamo tarehe 24/02/2021 Mkoa wa Geita uliwasilisha mapendekezo ya kuanzisha Wilaya mpya ya Busanda kwa kugawa maeneo ya Wilaya za Geita na Chato. Kwa kuwa mamlaka nyingi zilizoanzishwa bado zina upungufu wa miundombinu mbalimbali yakiwemo majengo ya utawala na huduma za kijamii, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuboresha miundombinu katika maeneo ya utawala yaliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itakapokamilisha maboresho ya miundombinu na huduma kwenye mamlaka zilizoanzishwa, itaendelea na taratibu za uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala ambayo yatakakidhi vigezo, ahsante.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Kizazi – Kibondo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa leo ni siku yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kwa takribani miezi mitatu tangu nipate changamoto za kiafya, naomba kwa dhati ya moyo wangu nitoe shukrani zifuatazo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, namshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aliyenijalia uhai, afya njema na kuniwezesha kurejea kuungana na Waheshimiwa Wabunge wenzangu katika kulijenga Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pili, kwa dhati ya moyo wangu, nitumie fursa hii ya Bunge tukufu kumshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo ameniwezesha kwa upendo wake na wema wake kwangu na Watanzania wote na kuniwezesha kupata matibabu na hatimaye kurejea kuendelea kulijenga Taifa letu. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais na tunamwombea sisi Watanzania aendelee kuwa na afya njema aendelee kuliongoza Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, nawashukuru sana Viongozi Wakuu wa Serikali, nikianza na Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ninamshukuru sana. Namshukuru sana Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Namshukuru sana kwa ushirikiano wake.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana wewe mwenyewe binafsi Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Spika wa viwango mwenye upendo. Ninakushukuru sana sana kwa ushirikiano wako na Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitumie fursa hii kumshukuru Bosi wangu, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Angellah Jasmine Kairuki, alikuwa nami muda wote na katika kila hatua ya matibabu yangu; na pia Mheshimiwa Naibu Waziri mwenzangu, Mheshimiwa Deo Ndejembi; Katibu Mkuu Ndunguru; na timu nzima ya Ofisi ya Rais TAMISEMI; ninawashukuru sana.

Mheshimiwa Spika, nawashukuru sana Mawaziri wote, Waheshimiwa Naibu Mawaziri wote na Waheshimiwa Wabunge wenzangu, nawashukuru sana, sana kwa upendo wenu na Mwenyezi Mungu awabariki sana kwa maombi yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru viongozi wangu wa Chama cha Mapinduzi wa Jimbo langu la Wanging’ombe, Baraza la Madiwani, viongozi wa Serikali, wananchi wenzangu wa Jimbo la Wanging’ombe kwa maombi yao siku zote. Niwahakikishie kwamba nitaendelea kuchapa kazi kuijenga Wanging’ombe na pia kujenga Taifa letu la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, namshukuru sana mke wangu mpenzi, Alafisa Moses Dugange kwa namna alivyokuwa karibu nami katika kipindi chote cha matibabu. Ninawashukuru sana, sana na Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, sasa naomba nianze kujibu maswali ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Johnson Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya katika Kata ya Kizazi Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo. Bajeti hiyo itatekeleza ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje (OPD), jengo la maabara, jengo la wazazi, jengo la upasuaji na jengo la kufulia, ahsante sana.
MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga soko na stendi ya kisasa eneo la Njiapanda Merya Halmashauri ya Wilaya ya Singida?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani, Mbunge wa Jimbo la Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Singida imeanza utekelezaji wa hatua za awali za ujenzi wa Stendi ya Njiapanda ya Merya. Katika mwaka wa fedha 2019/2020 halmashauri ilitenga kiasi cha shilingi milioni 10 na kufanya upimaji wa eneo la stendi, kufanya usafi na kusawazisha eneo.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali inakamilisha tathmini ya gharama za ujenzi wa stendi hiyo na kuanza kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2024/2025 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi. Halmashauri inaendelea na maandalizi ya andiko la mradi wa soko na litakapokamilika litawasilishwa Serikalini kwa ajili ya uchambuzi na endapo litakidhi vigezo litatengewa bajeti na kuanza ujenzi, ahsante.
MHE. ANNE K. MALECELA aliuliza: -

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu kadhia ya maji yanayotuama maeneo mengi wakati wa mvua katika Jiji la Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anne Kilango Malecela, Mbunge wa Jimbo la Same Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kudhibiti athari zinazotokana na mvua katika Jiji la Dar es Salaam; ikiwemo kujenga kingo za mito na mifereji mikubwa yenye urefu wa kilomita 30.7 kwa thamani ya shilingi bilioni 60 kupitia Mradi wa Uendelezaji Jiji la Dar es Salaam (DMDP).

Mheshimiwa Spika, kupitia Mradi wa DMDP awamu ya pili, Serikali inafanya usanifu na utambuzi wa maeneo kwa ajili ya ujenzi wa mifereji na mito yenye urefu wa kilomita 101.15, inayokadiriwa kutumia shilingi bilioni 200 katika wilaya zote za Mkoa wa Dar es Saalaam.

Mheshimiwa Spika, vilevile, TARURA kwa kushirikiana na Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) wanaendelea na ukamilishaji wa kazi ya ununuzi kwa ajili ya uboreshaji wa Mto Msimbazi, ikiwa ni jitihada za Serikali kuendelea kukabiliana na mafuriko katika Jiji la Dar es Salaam, ahsante.
MHE. MWANTUMU M. ZODO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga stendi za mabasi katika Halmashauri za Mkoa wa Tanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia mpando wa uboreshaji wa Majiji na Manispaa Tanzania TSCP imejenga Stendi ya Kisasa katika Jiji la Tanga na Halmashauri ya Mji wa Korogwe zilizogharimu takribani kiasi cha Shilingi billioni 10.7, ujenzi wa stendi hizo umekamilika na zinatumika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Katika mwaka wa fedha wa 2023/2024 Serikali imetenga bajeti ya shilingi billioni 10.312 kwa ajili ya uboreshaji wa miundombinu ya stendi katika halmashauri nchini. Aidha, Serikali itaendelea kujenga stendi za mabasi katika halmashauri kwa awamu kupitia programu mbalimbali kama, TACTIC, TSCP na vyanzo vingine yakiwemo mapato ya ndani ya halmashauri, ahsante. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Afya katika Kata ya Songambele ili kupunguza msongamano kwenye Kituo cha Afya Nkwenda Wilayani Kyerwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Jimbo la Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2021/2022, Serikali ilitenga bajeti ya shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Rutunguru katika Tarafa ya Kaisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya kwenye Kata za kimkakati kote nchini ikiwemo Kata ya Songambele iliyopo Halmashauri ya Wilaya ya Kyerwa, ahsante. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI K.n.y. MHE. TARIMBA G. ABBAS aliuliza: -

Je, Serikali haioni sasa ni wakati wa kuondoa sharti la kukopa kwa vikundi mikopo inayotolewa na Halmashauri?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeunda Timu ya Kitaifa kwa lengo la kupitia na kutoa mapendekezo ya namna bora ya kuratibu na kusimamia utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa. Timu hiyo imekalimisha jukumu hilo na kukabidhi taarifa Serikalini.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, Serikali inaendelea na uchambuzi na mapitio ya taarifa na pindi itakapokamilika taarifa rasmi itatolewa kwa Umma juu ya utaratibu wa mikopo ya asilimia 10 katika Mamlaka za Serikali za Mitaa, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO aliuliza: -

Je, lini Serikali itaanza ujenzi wa stendi ya kisasa kwenye eneo la Bondeni City Jijini Arusha kupitia Mradi wa TACTIC?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia mradi wa kuboresha miundombinu katika Majiji, Manispaa na Miji – TACTIC awamu ya pili, itatekeleza ujenzi wa stendi kuu ya kisasa ya mabasi katika eneo la Bondeni City, masoko mawili pamoja na bustani moja ya mapumziko kwa lengo la kuboresha huduma za kiuchumi na kijamii kwa wananchi wa Jiji la Arusha na maeneo jirani.

Mheshimiwa Spika, kazi ya usanifu imekamilika na taratibu za ununuzi kwa ajili ya kumpata mzabuni zinatarajiwa kukamilika mwezi Disemba, 2023. Baada ya taratibu hizo kukamilika, utekelezaji wa ujenzi kwenye maeneo yaliyoainishwa utaanza, ahsante.
MHE. INNOCENT E. KALOGERIS aliuliza:-

Je, lini Serikali itaiongezea fedha TARURA kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Jimbo la Morogoro Kusini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. NDUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Edward Kalogeris, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TARURA imeendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini. Bajeti ya utekelezaji wa miundombinu ya barabara imeongezeka kutoka kilometa 51.5 kwa shilingi milioni 660.95 kwa mwaka wa fedha 2020/2021 hadi kilometa 65.90 kwa shilingi bilioni 1.88 kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka wa fedha 2023/2024 jumla ya shilingi bilioni 2.2 zimetengwa kwa ajili ya ujenzi, ukarabati na matengenezo ya miundombinu ya barabara yenye urefu wa kilometa 85.9. Serikali itaendelea kuongeza bajeti kwa ajili ya uimarishaji wa miundombinu ya barabara katika Jimbo la Morogoro Kusini, ahsante. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI K.n.y. MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga barabara ya Mkuyuni hadi Mahandu kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing'oma Mabula, Mbunge wa Jimbo la Nyamagana, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara ya Mkuyuni hadi Mahandu ina urefu wa kilometa 10.5. Serikali imekamilisha usanifu kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami ambapo kiasi cha shilingi bilioni 20 zinahitajika. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali ilitenga shilingi billioni 5.36 kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya urefu wa kilometa 5.04 kiwango cha lami; kilometa 1.725 kiwango cha zege; kilometa 1.8 kiwango cha changarawe; na kilometa 0.7 kiwango cha mawe.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024, Serikali imetenga shilingi bilioni 3.42 kwa ajili ya ujenzi wa barabara kilometa 2.2 kiwango cha lami; kilometa 1.0 kiwango cha zege; kilometa 6.29 kwa kiwango cha changarawe; na kilometa 2.0 kiwango cha mawe.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuweka kwenye mpango Barabara ya Mkuyuni hadi Mahandu na barabara nyingine katika Jimbo la Nyamagana kwa kutenga bajeti kwa ajili wa ujenzi na matengenezo ya barabara hizo, ahsante. (Makofi)
MHE. HUSSEIN N. AMAR aliuliza:-

Je, lini Kituo cha Afya Kata ya Kafita na Zahanati ya Kijiji cha Nyijundu zitafunguliwa na kupelekewa vifaa baada ya ujenzi kukamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hussein Nassor Amar, Mbunge wa Jimbo la Nyang’hwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilitenga bajeti ya shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2020/2021 kwa ajili ya ujenzi katika Zahanati ya Nyijundu ambayo imepandishwa hadhi kuwa kituo cha afya. Ujenzi huo umekamilika na vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 120.4 vimepelekwa na huduma zimeanza kutolewa mwezi Aprili, 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa Kituo cha Afya Kafita unaendelea kwa fedha za TASAF shilingi milioni 500 ambapo majengo yanayojengwa ni jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje, jengo la maabara, jengo la wodi ya wazazi na jengo la upasuaji. Aidha, ujenzi wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje na maabara umekamilika na vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 120.4 vimepelekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri inaendelea na taratibu za ukamilishaji wa majengo yaliyobakia na huduma za awali zitaanza kutolewa kwenye majengo yaliyokamilika ifikapo mwezi Octoba mwaka 2023, ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU aliuliza:-

Je, lini Serikali itatoa fedha za ujenzi wa Kituo cha mabasi cha kisasa katika Halmashauri ya Wilaya Tunduru?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru iliwasilisha andiko la mradi wa ujenzi wa kituo cha mabasi. Baada ya kuchambuliwa andiko hilo halikukidhi vigezo hivyo lilirejeshwa Halmashauri kwa ajili ya kufanya maboresho na kuanza kutenga fedha kupitia mapato ya ndani kwa awamu kwa ajili ya ujenzi wa stendi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lililotengwa kwa ajili ya ujenzi wa stendi hiyo ya mabasi limekodishwa kwa Kampuni ya Kalpataru Power Transmissions Ltd inayofanya kazi ya ujenzi wa gridi ya Taifa kwa miaka miwili, (2022/2023 na 2023/2024). Hivyo, Ofisi ya Rais TAMISEMI inaielekeza Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru kukamilisha tathmini ya gharama za mradi na kuanza kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa stendi hiyo katika mwaka wa fedha 2024/2025, ahsante.
MHE. STANSLAUS H. NYONGO aliuliza: -

Je, lini jengo jipya la X-Ray litajengwa katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Haroon Nyongo, Mbunge wa Jimbo la Maswa Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia fursa ya mikopo inayotolewa na Mfuko wa Taifa wa Bima ya Afya (NHIF) inakamilisha taratibu za kupata mkopo wa shilingi milioni 190, kwa ajili ya ujenzi wa jengo la X–Ray katika Hospital ya Wilaya ya Maswa.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, kutokana na uchakavu wa baadhi ya majengo Serikali katika mwaka wa fedha 2023/2024 imetenga kiasi cha shilingi milioni 900, kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa majengo katika Hospitali ya Wilaya ya Maswa. Ahsante.
MHE. GEORGE N. MALIMA aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga vituo vya afya katika Kata za Mlembule, Godegode, Chunyu na Berege – Mpwapwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Jimbo la Mpwapwa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua mahitaji ya vituo vya afya katika Kata za kimkakati kote nchini. Katika kipindi cha miaka mitano Serikali imetekeleza ujenzi wa vituo vipatavyo 2,406 vya kutolea huduma za afya ambavyo bado vina uhitaji wa baadhi ya miundombinu ikiwemo vifaa tiba na watumishi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga kwa awamu fedha kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati kote nchini ikiwemo Kata za Godegode, Chunyu na Berege katika Halmashauri ya Mpwapwa, ahsante.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI aliuliza: -

Je, lini Serikali itafanya maboresho ya Sheria ya Mfuko wa Jimbo ili kuondoa kikwazo cha utekelezaji Zanzibar kwa kuwa Wabunge siyo Madiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Haji Kassim, Mbunge wa Mwanakwerekwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Mfuko wa Jimbo Na. 16 ya mwaka 2009, uidhinishwaji wa vipaumbele na matumizi ya fedha hufanywa na Kamati ya Mfuko wa Jimbo yenye wajumbe saba, akiwemo Mbunge wa Jimbo husika ambaye ndiye Mwenyekiti wa Kamati. Aidha, Kamati ina jukumu la kupokea, kujadili vipaumbele vya miradi iliyowasilishwa na wananchi na kuidhinisha miradi itakayotekelezwa.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Mfuko wa Kuchochea Maendeleo ya jimbo inatekelezwa sambamba na Sheria ya Fedha, Sheria ya Manunuzi ya Umma pamoja na Miongozo mbalimbali ya Mipango, Bajeti na Matumizi ya fedha za Umma. Hivyo, utaratibu uliopo kisheria unamwezesha Mbunge wa Jimbo husika kutimiza wajibu wake wa kupokea maombi, kuweka vipaumbele na kuidhinisha fedha kwa ajili ya utekelezaji wa vipaumbele vilivyokubaliwa, ahsante.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza: -

Je, lini Serikali itapeleka watumishi wa kutosha Wilayani Ludewa hususan eneo la elimu, afya na uvuvi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa ikama ya mwaka 2022/2023 Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa inahitaji jumla ya watumishi 3,327. Watumishi waliopo ni 1,985 hivyo kuwa na upungufu wa watumishi 1,342 sawa na asilimia 40.33.

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali iliajiri jumla ya wataalam 149 wa kada za afya, elimu msingi, sekondari na uvuvi na kuwapangia Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa. Serikali inatambua upungufu huo wa watumishi na itaendelea kuajiri wataalam wa kada mbalimbali na kuwapanga kwenye maeneo yenye mahitaji kote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa, ahsante.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, lini Serikali itaongeza posho za Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kazi kubwa inayofanywa na Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Vijiji katika kutoa huduma mbalimbali kwa wananchi. Kwa mujibu wa Sheria ya Mamlaka za Serikali za Mitaa Sura ya 290, kila halmashauri inatakiwa kuweka utaratibu wa kuwalipa posho, Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji kutoka katika vyanzo vya mapato ya ndani ya halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kutokana na changamoto za mapato kwenye halmashauri nyingi nchini, Serikali ilianza kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya kulipa posho za Waheshimiwa Madiwani pamoja na Wenyeviti wa vijiji.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 22.5 kwa ajili ya kulipa posho za Waheshimiwa Madiwani na Wenyeviti wa vijiji katika halmashauri 168.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuzijengea uwezo Mamlaka za Serikali za Mitaa ili ziweze kubuni na kuimarisha vyanzo vya mapato pamoja na kudhibiti mianya ya upotevu wa fedha kwa kutumia mifumo ya kieletroniki ya kukusanya na kutumia fedha katika kutekeleza miradi ya maendeleo pamoja na matumizi mengineyo ili kuongeza uwezo wa malipo kwa viongozi.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Hospitali mpya ya Wilaya ya Makete?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imeitenga shilingi milioni 900 kwa ajili ya kufanya ujenzi na ukarabati wa majengo ya Hospitali hiyo ili iweze kuwa na miundombinu bora yenye hadhi ya Hospitali ya Wilaya, ahsante.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara Jimbo la Serengeti hasa za vijijini ambazo hutumika kusafirishia mazao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jeremiah Mrimi Amsabi, Mbunge wa Jimbo la Serengeti, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Serengeti ina jumla ya mtandao wa barabara wenye urefu wa kilometa 971.78 zinazohudumiwa na TARURA. Barabara zenye hali nzuri ni kilometa 131.82, wastani kilometa 194.97 na mbaya ni kilometa 644.99. Katika mwaka wa fedha 2020/2021 barabara zenye urefu wa kilometa 121.24 zilifanyiwa matengenezo ya aina mbalimbali kwa gharama ya shilingi milioni 965.85.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 2.494 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilometa 152.24 ambazo ujenzi na matengenezo ya kilomita 138.74 za barabara na vivuko 34 yamekamilika. Matengenezo haya yanajumuisha barabara ya Mugumu – Masangula – Kemgesi kilometa 9.0, Kwitete – Mosongo – Wagete kilometa 25, Nyichoka – Maburi kilomita 6.0 na Barabara ya Nyamakobiti – Iselesele kilometa 7.1.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga fedha shilingi bilioni 2.41 kwa ajili ya ujenzi na matengenezo ya barabara zenye urefu wa kilomita 72.81 na vivuko vidogo 18.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la kubebea Wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mkalama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ina gari moja la kubebea wagonjwa ambalo lipo katika Hospitali ya Wilaya ya Mkalama na linahudumia Vituo vingine vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatapelekwa kwenye Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama. Ahsante.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa Vituo vya Afya Kata za Mundindi, Lupingu, Lupanga, Ludende, Madilu, Ludewa, Lugarawa na Mawengi utakamilika?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imekwishapeleka Shilingi Milioni 500 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa kwa ajili ya ukamilishaji wa Kituo cha Afya Mundindi kilichopo katika Kata ya Mundindi. Ujenzi wa jengo la la wagonjwa wa nje (OPD) na maabara umekwishakamilika na majengo mengine yapo kwenye hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeainisha maeneo ya kimkakati ya kujenga vituo vya afya katika Wilaya ya Ludewa kwa awamu kadri ya bajeti ya Serikali. Ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO K.n.y. MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je Serikali ina mpango gani wa kuunganisha barabara Kata za Ulaya, Kisanga, Malolo na Uleling’ombe katika Jimbo la Mikumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deniss Lazaro Londo Mbunge wa Jimbo la Mikumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali inaifanyia matengenezo barabara ya Kidodi – Vidunda yenye urefu wa kilomita 4.14 ambayo itawezesha uunganishaji wa Kata za Vidunda na Kidodi. Pia, ujenzi wa daraja la Ruhembe kwa gharama ya Shilingi Bilioni 1.00 utawezesha kuunganisha Kata za Ruhembe na Kidodi.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2022/2023, TARURA imetenga Shilingi Bilioni 1.00 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Ulaya – Kisanga kilomita 42.1 ambayo itaunganisha Kata za Ulaya na Kisanga. Aidha, kiasi cha Shilingi Milioni 500.00 zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa daraja la Ruhembe linalounganisha Kata za Ruhembe na Kidodi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kuunganisha Kata ya Malolo na Uleling’ombe katika Jimbo la Mikumi kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA K.n.y. MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga vituo vya afya katika Jimbo la Lupembe ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Jimbo la Lupembe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka na imekwishaanza kutekeleza mpango wa kujenga vituo vya huduma za afya katika Jimbo la Lupembe.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali ilitenga shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya kuboresha miundombinu ya afya katika Jimbo la Lupembe. Aidha, hadi kufikia tarehe 30 Mei, 2022 imekwishapeleka shilingi bilioni 1.5 ambapo shilingi milioni 550 kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya vya Ikondo na Kitiwa; shilingi milioni 150 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati tatu za Ihang’ana, Maduma na Lyalalo; na shilingi milioni 800 kwa ajili ukarabati wa miundombinu ya Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Njombe. Ahsante.
MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuajiri watumishi wa kutosha katika kada za afya na elimu nchini?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKAO NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. NDUGAGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweka mkakati wa kuendelea kuajiri watumishi wa kada za afya na elimu kwa awamu kwa kutenga vibali vya ajira katika bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuajiri watumishi wa kada ya afya na elimu kwa awamu na katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepanga kuajiri watumishi 7,612 wa kada ya afya na watumishi 9,800 wa kada ya ualimu katika halmashauri zote nchini. Ahsante.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la kubebea Wagonjwa katika Hospitali ya Wilaya ya Mkalama?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama ina gari moja la kubebea wagonjwa ambalo lipo katika Hospitali ya Wilaya ya Mkalama na linahudumia Vituo vingine vya kutolea huduma za afya.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatapelekwa kwenye Halmashauri zote nchini ikiwemo Halmashauri ya Wilaya ya Mkalama. Ahsante.
MHE. JOSEPH Z. KAMONGA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa Vituo vya Afya Kata za Mundindi, Lupingu, Lupanga, Ludende, Madilu, Ludewa, Lugarawa na Mawengi utakamilika?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Zacharius Kamonga, Mbunge wa Jimbo la Ludewa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imekwishapeleka Shilingi Milioni 500 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Ludewa kwa ajili ya ukamilishaji wa Kituo cha Afya Mundindi kilichopo katika Kata ya Mundindi. Ujenzi wa jengo la la wagonjwa wa nje (OPD) na maabara umekwishakamilika na majengo mengine yapo kwenye hatua mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeainisha maeneo ya kimkakati ya kujenga vituo vya afya katika Wilaya ya Ludewa kwa awamu kadri ya bajeti ya Serikali. Ahsante.
MHE. FLORENT L. KYOMBO K.n.y. MHE. DENNIS L. LONDO aliuliza: -

Je Serikali ina mpango gani wa kuunganisha barabara Kata za Ulaya, Kisanga, Malolo na Uleling’ombe katika Jimbo la Mikumi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deniss Lazaro Londo Mbunge wa Jimbo la Mikumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali inaifanyia matengenezo barabara ya Kidodi – Vidunda yenye urefu wa kilomita 4.14 ambayo itawezesha uunganishaji wa Kata za Vidunda na Kidodi. Pia, ujenzi wa daraja la Ruhembe kwa gharama ya Shilingi Bilioni 1.00 utawezesha kuunganisha Kata za Ruhembe na Kidodi.

Mheshimiwa Spika, Katika mwaka wa fedha 2022/2023, TARURA imetenga Shilingi Bilioni 1.00 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Ulaya – Kisanga kilomita 42.1 ambayo itaunganisha Kata za Ulaya na Kisanga. Aidha, kiasi cha Shilingi Milioni 500.00 zimetengwa kwa ajili ya ukamilishaji wa daraja la Ruhembe linalounganisha Kata za Ruhembe na Kidodi.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kuunganisha Kata ya Malolo na Uleling’ombe katika Jimbo la Mikumi kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza: -

Je, ni lini Kata ya Kwihancha itapata Kituo cha Afya na ni lini huduma za afya zitaimarishwa katika Hospitali ya Nyamwaga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita Mwikwabe Waitara, Mbunge wa Jimbo la Tarime Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022, imetenga Shilingi Milioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa Jengo la Wagonjwa wa Nje (OPD) na Maabara katika kituo cha afya. Fedha hiyo itapelekwa kabla ya tarehe 30 Juni, 2022. Aidha katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi Milioni 400 kwa ajili ya kuendeleza ujenzi wa kituo hicho.

Mheshimiwa Spika, huduma za afya katika Hospitali ya Nyamwaga zinaendelea kuimarika ambapo Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022, imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa hospitali hiyo. Ujenzi wa wodi mbili za wanaume na wanawake umekamilika na ujenzi wa majengo ya maabara, wodi ya watoto na jengo la kuhifadhia dawa upo katika hatua za umaliziaji. Aidha, huduma zinaendelea kutolewa ikiwemo huduma za uzazi na upasuaji.
MHE. GHATI Z. CHOMETE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya ukarabati wa Stendi Kuu ya Mabasi Bweri iliyopo Manispaa ya Musoma?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ghati Zephania Chomete, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Stendi ya Mabasi ya Bweri katika Manispaa ya Musoma ilijengwa mwaka 2007 kwa mapato ya ndani ya halmashauri kwa kutumia Mkandarasi CMG Construction Company Limited aliyeingia Mkataba wa shilingi bilioni 1.36 ambapo Mkandarasi huyo alifanya kazi zenye thamani ya shilingi milioni 921.17.

Mheshimiwa Spika, lengo la Serikali ilikuwa kujenga stendi hiyo kupitia ufadhili wa Benki ya Kiarabu ya Maendeleo ya Afrika (BADEA). Hata hivyo kutokana na majadiliano kutozaa matunda, Serikali imeiweka stendi hiyo kwenye Mpango wa TACTIC ambapo shilingi bilioni 1.35 zimetengwa.
MHE. ZAINAB A. KATIMBA K.n.y MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Je, Serikali ina kauli gani kuhusu mikopo inayotolewa na Halmashauri kwa kuwa mfumo unawaacha nje vijana wengi kwa kukosa sifa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kanuni ya 6 ya Kanuni za Utoaji na Usimamizi wa Mikopo ya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu ya Mwaka 2018 pamoja na marekebisho yake inaelekeza sifa na vigezo vya kuzingatiwa kwenye utoaji mikopo kwa vijana.

Mheshimiwa Spika, vigezo na sifa hizo ni pamoja na kikundi kinachofanya shughuli za ujasiriamali au kinachotarajia kuanza shughuli hizo, Kikundi kiwe kimetambuliwa kama kikundi cha vijana; Wanakikundi wawe Watanzania wenye umri kati ya miaka 18 hadi 35; Kikundi cha vijana kiwe na idadi ya wanakikundi kuanzia watano (5) na kuendelea; Kikundi kiwe na akaunti ya benki iliyofunguliwa kwa jina la kikundi kwa ajili ya matumizi ya kikundi; na Kikundi hakitajumuisha wajumbe wenye ajira rasmi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia sifa hizo, katika mwaka wa fedha 2021/2022, jumla ya Vikundi 1,441 vya Vijana vilikopeshwa mikopo yenye thamani ya shillingi Bilioni 13.5 nchini kote.

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali ni kwamba, vijana wenye sifa tajwa waendelee kujiunga katika vikundi vya wajasiriamali na kuomba mikopo hiyo ili kuinua uchumi wao. Ahsante.
MHE. STELLA I. ALEX aliuliza: -

Je, ni Halmashauri na Manispaa ngapi nchini zinatekeleza ununuzi na ugawaji wa mafuta ya ngozi kwa watu wenye ulemavu wa ngozi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Alex Ikupa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, huduma kwa watu wenye ulemavu zimeendelea kuboreshwa kote nchini, ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 jumla ya watu wenye ulemavu 138,468 kati yao wanawake 68,401 na wanaume 70,067 wametambuliwa. Aidha, katika kipindi hicho, watu wenye ulemavu wapatao 15,596 wamehudumiwa kwa gharama ya shilingi bilioni 1.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuwakinga watu wenye ualbino dhidi ya maradhi ya ngozi kutokana na jua, kati ya mwaka 2020 hadi 2022 jumla ya Halmashauri 102 kwenye mikoa 20 imetekeleza ununuzi na ugawaji wa mafuta ya ngozi (sun-screen cream) kwa kushirikiana na wadau. Jumla ya wanufaika 3,389 walipata huduma hiyo. Ahsante.
MHE. HASSAN Z. KUNGU aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka shilingi milioni 500 ya ujenzi wa Kituo cha Afya Namiungo na shilingi milioni 200 ya Kituo cha Afya cha Nakayaya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/23 Serikali imetenga shilingi milioni 400 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya Nakayaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kujenga Vituo vya Afya kwenye Kata za kimkakati kwa awamu ikiwemo Kata ya Namiungo. Ahsante.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA K.n.y. MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Jengo jipya la Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Jimbo la Biharamulo Magharibi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo, mwezi Februari, 2022 iliwasilisha maombi maalum ya shilingi bilioni 3.475 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la utawala la Halmashauri. Maombi hayo yaliwasilishwa nje ya muda ambapo ukomo wa bajeti kwa mwaka 2022/2023 ulikuwa umeshatolewa hivyo kushindwa kutengwa kwa bajeti hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 itatenga kiasi cha shilingi bilioni 2.7 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Biharamulo kwa kuwa ni kiasi ambacho kimewekwa na Wizara kwa ujenzi wa majengo ya Halmashauri. Ahsante.
MHE. SELEMANI J. ZEDI aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kuipandisha hadhi Zahanati ya Kijiji cha Sojo ili kiwe Kituo cha Afya na kuweza kuhudumia wananchi na watumishi wa Mradi wa Bomba la Mafuta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Selemani Jummane Zedi, Mbunge wa Jimbo la Bukene kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Sojo ni moja kati ya vijiji saba vya Kata ya Igusule yenye wakazi 23,237. Kata hii ina zahanati moja iliyopo katika Kijiji cha Sojo ambayo inaendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha afya kwenye Kata ya Igusule.
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa stendi ya kisasa ya mabasi katika Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Pius Stephen Chaya, Mbunge wa Jimbo la Manyoni Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni imekwishaandaa wazo mradi (concept note) kwa ajili ya ujenzi wa Mradi wa kimkakati wa stand ya mabasi. Kazi inayoendelea kwa sasa ni kutafuta msanifu wa mradi kwa ajili ya kuandaa michoro ambayo itawezesha kujua gharama halisi za mradi huo. Kazi hii ya usanifu inatarajiwa kukamilika ifikapo tarehe 30 Juni, 2022.

Mheshimiwa Spika, baada ya kupata gharama halisi za mradi huo na kukidhi vigezo vya mradi wa kimkakati, Serikali itatafuta fedha kwa ajili ya kuutekeleza. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa maboma ya zahanati ya Kimu, Rofat, Tumbakose, Songolo na Sori Wilayani Chemba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Jimbo la Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepeleka shilingi milioni 260 kwa ajili ya ukamilishaji wa zahanati 6 za Jangalo, Wairo, Humekwa, Makamaka na Ombiri. Ujenzi wa zahanati hizi umefikia hatua za umaliziaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga Shilingi milioni 200 kwa ajili ya kukamilisha Zahanati za Nkulari, Nkikima, Mlongia na Handa. Aidha, ujezi wa maboma ya zahanati ya Rofat, Tumbakose na Songolo ambazo zinajengwa kwa nguvu za wananchi bado hazijafika hatua ya lenta ili kupata fedha ya Serikali kwa ajili ya ukamilishaji.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha Kituo cha Afya Mtina ili kiweze kutoa huduma ya upasuaji pamoja kupeleka vifaatiba katika Kituo cha Afya Mchoteka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi millioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji, jengo la mama na mtoto na maabara katika Kituo cha Afya cha Mtina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi bilioni 47.7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa ajili ya vituo vya afya 159 ambavyo vimekamilika ikiwa ni pamoja na Kituo cha Afya Mchoteka, ahsante.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaboresha Kituo cha Afya Mtina ili kiweze kutoa huduma ya upasuaji pamoja kupeleka vifaatiba katika Kituo cha Afya Mchoteka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Jimbo la Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi millioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa jengo la upasuaji, jengo la mama na mtoto na maabara katika Kituo cha Afya cha Mtina.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imetenga shilingi bilioni 47.7 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa ajili ya vituo vya afya 159 ambavyo vimekamilika ikiwa ni pamoja na Kituo cha Afya Mchoteka, ahsante.
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA aliuliza: -

Je, ni kiasi gani Halmashauri zinahakikisha 30% ya fedha za manunuzi zinakwenda kwenye kampuni za wanawake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Ununuzi wa Umma ya mwaka 2011 inaekeleza taasisi nunuzi zote kutenga asilimia 30 ya bajeti inayotengwa katika manunuzi kwa ajili ya makundi maalum ambayo ni makundi ya vijana, wanawake, wazee na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Spika, mpaka kufikia Mei, 2022 jumla ya Halmashauri 24 kati ya 184 zimekwishavitambua na kuwezesha usajili wa vikundi 88 katika Mamlaka ya Kudhibiti Manunuzi ya Umma (PPRA) ikiwa ni kigezo cha lazima cha kisheria cha kuwezesha kundi hilo maalum kupata zabuni za ununuzi.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kuzielekeza Halmashauri zote nchini kuhamasisha vikundi kujisajili na kutenga kiwango cha asilimia 30 ya bajeti ya manunuzi kwa vikundi hivyo vikiwemo vikundi vya wanawake. (Makofi)
MHE. ALLY J. MAKOA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka gari la wagonjwa katika Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Kondoa?

NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Juma Makoa, Mbunge wa Jimbo la Kondoa Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatapelekwa kwenye Halmashauri 184 nchini kote ikiwemo Halmashauri ya Mji wa Kondoa. Ahsante.
MHE. MINZA S. MJIKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka mtaalam wa X–Ray katika Hospitali ya Wilaya ya Meatu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 inaajiri watumishi 7,612 wa kada mbalimbali za afya, wakiwemo wataalam wa X-Ray. Hivyo, Hospitali ya Wilaya ya Meatu itapatiwa mtaalam wa X-ray baada ya taratibu za ajira kukamilika, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. DEO K. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Kituo cha Afya Makambako kitapata mashine ya X-ray na Ultra Sound?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishapeleka mashine ya X-ray kwenye Kituo cha Afya Makambako ambayo ilisimikwa kituoni hapo mwezi Machi, 2021 na inatumika.

Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba 2021 Serikali ilipeleka mashine ya Ultrasound katika Kituo cha Afya cha Makambako na inatumika, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE K.n.y. MHE. DEO K. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Kituo cha Afya Makambako kitapata mashine ya X-ray na Ultra Sound?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Jimbo la Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekwishapeleka mashine ya X-ray kwenye Kituo cha Afya Makambako ambayo ilisimikwa kituoni hapo mwezi Machi, 2021 na inatumika.

Mheshimiwa Spika, mwezi Septemba 2021 Serikali ilipeleka mashine ya Ultrasound katika Kituo cha Afya cha Makambako na inatumika, ahsante.
MHE. CHARLES M. KAJEGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha majengo ya shule na zahanati ambayo yalijengwa kwa nguvu za wananchi katika Jimbo la Mwibara?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Charles Muguta Kajege, Mbunge wa Jimbo la Mwibara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imetenga shilingi milioni 287.5 kwa ajili ya ukamilishaji wa vyumba vya madarasa 14 katika Halmashauri ya Wilaya ya Bunda. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/2023 Serikali imetenga shilingi milioni 240 kwa ajili ya kukamilisha vyumba vya madarasa 14 katika Jimbo la Mwibara pamoja na ukamilishaji wa maabara tatu za kemia, baiolojia na fizikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma ya zahanati. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imekwisha peleka kwenye Jimbo la Mwibara shilingi milioni 100 kwa ajili ya kukamilisha maboma mawili ya zahanati za Sozia na Ragata. Aidha, katika mwaka wa fedha 2022/23 shilingi milioni 88 imetengwa kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati ya Nyamitwebiri.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga stendi kuu ya mabasi Bukoba Mjini?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti wa Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2017/2018, 2018/2019 na 2019/2020 Serikali ilipeleka jumla ya shilingi milioni 835.95 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa stendi mpya ya mabasi katika eneo la Kyakailabwa Kata ya Nyanga. Fedha hizo zilitumika kwa ajili ya ujenzi wa barabara ya kuingilia stendi kwa kiwango cha lami, ujenzi wa vyoo, ujenzi wa mabanda matatu ya abiria na kituo cha polisi umekamilika. Aidha, ujenzi wa eneo la maegesho ya mabasi na malori upo hatua ya changarawe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imejumuisha mradi wa stendi hiyo kwenye Mpango wa TACTIC awamu ya pili. Ahsante.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatimiza ahadi yake ya kuboresha na kupanua Vituo vya Afya vya Bungu, Magama na Mombo ambavyo vinahudumia wananchi wengi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Jimbo la Korogwe Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza ujenzi wa vituo vya afya kote nchini ikiwemo katika Jimbo la Korogwe Vijijini. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali imepeleka shilingi milioni 800 kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya Mnyuzi na Kerenge katika Jimbo la Korogwe Vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Vituo vya Afya vya Mombo, Bungu na Magoma Serikali inafanya tathmini ya vigezo stahiki kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya utekelezaji.
MHE. ERIC J. SHIGONGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapandisha hadhi Zahanati ya Maisome kuwa Kituo cha Afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eric James Shigongo, Mbunge wa Jimbo la Buchosa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa miongozo ukubwa wa eneo la kituo cha afya linatakiwa kuwa na angalau ekari nne katika maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Spika, Serikali haikuipandisha hadhi Zahanati ya Maisome iliyopo Kijiji cha Kanoni kuwa Kituo cha Afya kwa sababu ya kukosa eneo la ujenzi. Aidha, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 imepeleka shilingi milioni 500 kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Buchosa kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya kwenye Kata ya Maisome, Kijiji cha Kanoni. Ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje na jengo la maabara upo katika hatua ya ukamilishaji na ujenzi wa majengo ya wodi ya wazazi, jengo la upasuaji, jengo la kufulia na kichomea taka upo hatua ya awali, ahsante.
MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Kituo cha Afya katika Kata za Luguru na Sawida Wilayani Itilima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa vituo vya afya katika kata za kimkakati zenye idadi kubwa ya watu na umbali mrefu kutoka kituo cha karibu cha huduma.
Mheshimiwa Spika, katika kipindi cha mwaka wa fedha 2021/2022 hadi Septemba 2023, jumla ya vituo vya afya 348 vimejengwa nchini kote. Kazi ya ujenzi huu ni endelevu hivyo tathmini ya vigezo kwa Kata za Luguru na Sawida itafanyika na kuingizwa kwenye mipango ya ujenzi, ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Wodi ya Akinamama, Watoto na Wanaume katika Vituo vya Afya Lukungu - Lamadi na Kiloleli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Vituo vya Afya vya Lukungu na Kiloleli ni miongoni mwa vituo vilivyosajiliwa na kuanza kutoa huduma vikiwa na upungufu wa miundombinu ikiwemo Wodi ya Wazazi, Jengo la Upasuaji na Maabara.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa awamu kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa miundombinu inayopungua kwenye vituo vya afya kote nchini vikiwemo Vituo vya Afya vya Lukungu na Kiloleli, ahsante.
MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza:-

Je, upi Mkakati wa kuwapa kipaumbele cha ajira walimu wanaojitolea katika shule za msingi na sekondari pindi ajira zinapotoka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Jimbo la Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imeandaa mwongozo wa kuwatambua Walimu wanaojitolea katika shule zote nchini. Mwongozo huo umeipa Ofisi ya Rais, TAMISEMI jukumu la kuandaa mfumo wa Walimu wanaojitolea. Kwa sasa mfumo huo unaendelea kuandaliwa, utakapokamilika Walimu watajulishwa ili waanze kufuata utaratibu wa kujisajili katika mfumo huo ili kurahisisha utambuzi wao, ahsante.
MHE. ORAN M. NJEZA K.n.y. MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza: -

Je, ni lini Mamlaka ya Mji Mdogo wa Rujewa inaenda kuwa Mamlaka kamili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Jimbo la Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mhesimiwa Naibu Spika, kwa mujibu wa Sheria ya Serikali za Mitaa (Mamlaka za Miji) Sura 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa Mwaka 2014, vigezo na taratibu zinazopaswa kufuatwa ni pamoja na maombi rasmi kuwasilishwa Ofisi ya Rais TAMISEMI. Ofisi ya Rais TAMISEMI itakapopokea maombi rasmi ya Halmashauri ya Mji Mbarali itafanya uchambuzi na tathmini ya kukidhi vigezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo kumekuwa na changamoto za uendeshaji na tija za kuwepo kwa baadhi ya Mamkaka za Miji Midogo. Ofisi ya Rais TAMISEMI inafanya uchambuzi na kubaini tija ya kuendelea kuwepo au la, kwa baadhi ya Mamlaka za Miji Midogo.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je ni lini ahadi ya Rais wa Awamu ya Tano ya kuipandisha hadhi Shule ya Sekondari Nassa itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Mwongozo wa Uanzishaji na Usajili wa Shule wa Mwaka 2020 uliotolewa na Wizara ya Elimu unabainisha hatua za kuipandisha hadhi shule kuwa ya Kidato cha Tano na Sita kama ifuatavyo: -

Mwombaji ambae ni Mkurugenzi ataandika barua kwa Kamishna wa Elimu kupitia Mdhibiti Mkuu wa Ubora wa Shule Kanda. Barua hiyo itaambatishwa na taarifa ya ukaguzi wa Mdhibiti wa Ubora wa Shule Kanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega kutenga fedha kupitia mapato ya ndani ili kukamilisha miundombinu muhimu inayowezesha shule hii kukidhi vigezo vya kupandishwa hadhi ya kuwa na Kidato cha Tano na cha Sita.
MHE. HAMIS M. MWINJUMA K.n.y MHE. JACQUELINE K. ANDREA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa fedha kukamilisha ujenzi wa Shule katika Kijiji cha Izengabatogilwe, Kata ya Ugalla - Urambo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaqueline Andrea Kainja, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 imepeleka Shilingi Milioni 40 kwa ajili ya ujenzi wa vyumba viwili vya madarasa katika kitongoji cha Gimagi kwenye shule shikizi ya shule Mama ya Izengabatogile.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga Shilingi Milioni 220 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa yaliyojengwa kwa nguvu za wananchi katika Halmashauri ya Wilaya ya Urambo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa ikiwemo ya shule katika Kijiji cha Izengabatogile, Kata ya Ugalla, Wilayani Urambo.
MHE. MINZA S. MJIKA aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga Zahanati katika Kata ya Binza – Maswa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Minza Simon Mjika, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Mwongozo wa Ujenzi wa Zahanati katika Mpango wa Maendeleo ya Afya ya Msingi (MMAM) wa mwaka 2007 wananchi wanatakiwa kuanza ujenzi wa boma mpaka hatua ya lenta.

Mheshimiwa Spika, baada ya kufikia hatua ya lenta Serikali hupeleka fedha kwa ajili ya umaliziaji wa jengo. Hivyo wananchi wa Kata ya Binza wanashauriwa kuanza kwa utaratibu huo, ahsante.
MHE. EDWIN E. SWALLE aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kupeleka Watumishi, Vifaa Tiba na Tendanishi kwenye Vituo vya Afya na Zahanati katika Jimbo la Lupembe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edwin Enosy Swalle, Mbunge wa Jimbo la Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imetenga shilingi milioni 700 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa ajili ya hospitali, vituo vya afya na zahanati katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023, Serikali imepeleka jumla ya watumishi 72 wa Kada mbalimbali za afya kwa ajili ya kutoa huduma katika Halmashauri ya Wilaya ya Njombe.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti ya ununuzi wa vifaa tiba pamoja na kuajiri watumishi wa kada mbalimbali za afya kwa ajili ya kwenda kutoa huduma kwenye vituo kote nchini, ahsante.
MHE. OMARI M. KIGUA aliuliza: -

Je, lini Serikali itatoa fedha kukamilisha ujenzi wa majengo ya zahanati Kijiji cha Masagalu Mission, Kilindi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omari Mohamed Kigua, Mbunge wa Jimbo la Kilindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 Serikali ilipeleka shilingi milioni 100 katika Halmashauri ya Kilindi kwa ajili ya kukamilisha boma la Zahanati ya Masagalu. Kwa kuwa boma hilo lilijengwa kwa ramani ya zamani ambayo ni kubwa zaidi, ujenzi haukuweza kukamilika.

Mheshimiwa Spika, Zahanati ya Masagalu imeanza kutoa huduma kwenye baadhi ya vyumba ambavyo vimekamilika. Aidha, Serikali kupitia Mapato ya ndani ya Halmashauri ya Kilindi itatenga shilingi millioni 100 katika Mwaka wa Fedha 2024/2025 ili kukamilisha ujenzi, ahsante.
MHE. ZAYTUN S. SWAI aliuliza: -

Je, lini Serikali itajenga Jengo la Mama na Mtoto kwenye Kituo cha Afya – Loliondo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaytun Seif Swai, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Loliondo ni moja ya Vituo vya Afya chakavu 199 vilivyoainishwa na Ofisi ya Rais – TAMISEMI kwa ajili ya upanuzi. Aidha, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati pamoja na kuongeza miundombinu mbalimbali ikiwemo majengo ya Mama na Mtoto yenye uwezo wa kutoa huduma ya upasuaji wa dharura. Ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza mgogoro wa mpaka kati ya Handeni na Kilindi katika eneo la Bondo?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kwagilwa Reuben Nhamanilo, Mbunge wa Jimbo la Handeni Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwisha tatua mgogoro wa mpaka kati ya Halmashauri ya Mji wa Handeni na Kilindi katika eneo la Bondo kwa maelekezo yaliyotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Tanga kwenye kikao cha tarehe 25 Julai, 2023.

Mheshimiwa Spika, timu ya wataalam wa ardhi, Wajumbe wa Kamati za Ulinzi na Usalama wa Wilaya na viongozi ngazi ya Tarafa, Kata na Vijiji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kilindi na Handeni walikutana tarehe 8 – 9 Oktoba, 2021 kwa ajili ya kupitia Tangazo la Serikali (GN), kuhakiki idadi ya watu, kuhakiki upatikanaji wa huduma za kijamii pamoja na kutoa ushauri wa kitaalam ambapo taarifa hiyo iliwasilishwa Ofisi ya Mkuu wa Mkoa kwa utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, Wakurugenzi wa halmashauri ya Kilindi na Handeni wameelekezwa kutekeleza masuala yafuatayo; kuendelea kutoa elimu kwa wananchi juu ya umuhimu wa uhifadhi wa misitu, kuheshimu mpaka ulioainishwa kutokana na tafsiri sahihi ya matangazo ya Serikali, kurekebisha usajili wa shule za Msingi Bondo na Parakwiyo ili zisomeke ndani ya Wilaya husika, ahsante.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza changamoto ya upungufu wa Watumishi wa Kada ya Afya katika Vituo ya Afya Karatu Mjini na Kaloleni – Arusha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Catherine Valentine Magige, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 na 2022/2023 Serikali imeajiri na kuwapangia vituo watumishi 83 wa kada mbalimbali za afya katika Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, na watumishi 79 katika Halmashauri ya Jiji la Arusha. Aidha, watumishi 14 walipangwa katika kituo cha afya Karatu Mjini na watumishi 18 katika kituo cha afya Kaloleni Halmashauri ya Jiji la Arusha.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kuajiri wataalam wa kada mbalimbali za Afya na kuwapanga katika vituo vyenye upungufu mkubwa kote nchini, zikiwemo halmashauri za Karatu na Jiji la Arusha.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Je, lini Serikali itatimiza ahadi ya kupeleka majokofu manne ya mochwari kwenye Kituo cha Afya Mugeta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa vifaatiba ikiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti katika vituo vya huduma za afya. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali ilitenga na kupeleka shilingi milioni 700 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa Halmashauri ya Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya fedha hizo, kiasi cha shilingi milioni 32.7 kimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa jokofu moja la milango sita la Kituo cha Afya cha Mugeta. Taratibu za manunuzi zinafanyika kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD) na inatarajiwa kukamilika kati ya mwezi huu Februari na Machi 2024. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza:-

Je, lini Serikali itamalizia ujenzi wa zahanati ya Uwanja wa Ndege katika Kata ya Mafisa Mkoani Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kusogeza huduma za afya kwa wananchi wa Uwanja wa Ndege, mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilipeleka shilingi milioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati ya Uwanja wa Ndege iliyopo katika Kata ya Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro. Ujenzi umekamilika na huduma zimeanza kutolewa mwezi Mei, mwaka 2022. Zahanati hii kwa wastani huhudumia wagonjwa wapatao 750 kwa mwezi na wagonjwa 9,000 kwa mwaka, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE aliuliza: -

Je, lini Serikali itakamilisha Ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Ngerengere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamisi Shabani Taletale, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Ngerengere kilisajiliwa mwezi Mei, 1995 na kinatoa huduma ya ngazi ya Kituo cha Afya ikiwa ni pamoja na huduma za upasuaji wa dharura na huduma nyingine. Aidha, kituo hiki kinahudumia wastani wa wagonjwa 1,200 kwa mwezi na 14,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hiki kina upungufu wa baadhi ya miundombinu ikiwemo jengo la Huduma za Mama na Mtoto na Upasuaji, jengo la Maabara, jengo la kuhifadhia maiti na jengo la kufulia. Eneo la Kituo hicho lina ukubwa wa ekari nne na nusu, hivyo halitoshelezi mahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, inaendelea kufanya mazungumzo na Shirika la Posta ambalo linamiliki eneo mkabala lenye ukubwa wa ekari mbili ambalo halijaendelezwa ili litumike kupanua Kituo cha Afya cha Ngerengere, ahsante.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza: -

Je, kuna mpango gani kuruhusu Kata za Kanindo, Igombemkulu na Milambo kufanya Uchaguzi wa Serikali za Mitaa na Udiwani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Jimbo la Ulyankulu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa Kata za Kanindo, Igombemkulu na Milambo katika Halmashauri ya Wilaya ya Kaliua. Hata hivyo, maeneo hayo bado yana mwingiliano wa makazi ya wakimbizi na raia, hali ambayo huathiri utekelezaji wa shughuli za uchaguzi ndani ya maeneo hayo. Serikali inaendelea kushughulikia suala hili chini ya Ofisi ya Rais TAMISEMI na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ili kuhakikisha wananchi wa Kata hizo wanapata haki ya kushiriki kwenye shughuli za uchaguzi.


MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI aliuliza: -

Je, lini Serikali itakarabati Kituo cha Afya cha Kifura – Muhambwe?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Florence George Samizi, Mbunge wa Jimbo la Muhambwe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Kifura kilichopo Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo ni moja ya vituo vya afya 199 chakavu ambavyo Ofisi ya Rais TAMISEMI imeviainisha. Serikali inaendelea kutenga bajeti kwa ajili ya ukarabati na kuongeza majengo kwenye vituo vya afya chakavu vyote nchini kikiwemo Kituo hiki cha Afya cha Kifura, ahsante.

MHE. VITA R. KAWAWA aliuliza:-

Je, lini Serikali itapeleka Walimu kukidhi mahitaji katika Shule za Sekondari na Msingi Wilayani Namtumbo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, Mbunge wa Jimbo la Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiajiri walimu wa Shule za Msingi na Sekondari kwa awamu kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha. Katika mwaka wa fedha 2022/2023 na 2021/2022, Serikali iliajiri walimu 22,930 ambapo walimu 111 walipangiwa katika shule zilizopo kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali itaendelea kupeleka walimu kwenye Shule za Msingi na Sekondari zikiwemo zilizopo katika Wilaya ya Namtumbo kulingana na uhitaji lakini pia kulingana na upatikanaji wa fedha, ahsante.

MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakarabati Jengo la OPD na kujenga uzio katika Kituo cha Afya Likombe - Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Likombe ni moja ya vituo vya afya vilivyonufaika na mpango wa maboresho ambapo katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, kituo hicho kilipokea shilingi milioni 500 na kujenga jengo la wazazi, maabara, jengo la kuhifadhia maiti, stoo ya dawa, nyumba ya mtumishi na kichomea taka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na maboresho makubwa yaliyofanywa katika kituo hicho, bado kuna uhitaji wa jengo la kuhudumia wagonjwa wa nje (OPD) pamoja na uzio.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka wa fedha 2024/2025, Serikali kupitia mapato ya ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara itatenga shilingi milioni 70 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa jengo la wagonjwa wa nje katika Kituo cha Afya cha Likombe. Ahsante. (Makofi)
MHE. OMAR ISSA KOMBO aliuliza:-

Je, Serikali inazingatia vigezo gani kugawa fedha za Mfuko wa Jimbo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Omar Issa Kombo, Mbunge wa Jimbo la Wingwi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mfuko wa Jimbo umeanzishwa kwa mujibu wa Sheria Na. 16 ya mwaka 2009 kwa lengo la kuwawezesha Waheshimiwa Wabunge kuchochea maendeleo ya Jimbo. Aidha, vigezo vinavyotumika kugawa fedha za mfuko wa Jimbo ni pamoja na idadi ya watu Jimboni asilimia 45, mgao sawa kila Jimbo asilimia 25, kiwango cha umaskini asilimia 20 na ukubwa wa eneo asilimia10, ahsante.
MHE. JOSEPH A. TADAYO aliuliza:-

Je, lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa Stendi ya kisasa katika Mji wa Mwanga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Anania Tadayo, Mbunge wa Jimbo la Mwanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua changamoto ya ufinyu wa stendi ya magari katika Halmashauri ya Mwanga. Halmashuri imeandaa andiko lenye thamani ya shillingi bilioni 3.2 kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya kisasa na kuliwasilisha Ofisi ya Rais, TAMISEMI mwezi Agosti, 2023 ambapo wataalam wanaendelea na mapitio ya andiko hilo kulingana na vigezo kwa ajili ya utekelezaji, ahsante.
MHE. SUMA I. FYANDOMO K.n.y. MHE. KASALALI E. MAGENI aliuliza:-

Je, lini Serikali itakamilisha mchakato wa kuanzisha Halmashauri ya Wilaya ya Sumve ili kusogeza huduma kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kasalali Emmanuel Mageni, Mbunge wa Jimbo la Sumve, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala upo kwa mujibu wa Sheria za Serikali za Mitaa Sura ya 287 na 288 pamoja na Mwongozo wa Uanzishwaji wa Maeneo ya Utawala wa Mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, maombi ya kuanzisha Halmashauri mpya yanatakiwa kujadiliwa, kuridhiwa na kupitishwa kwenye vikao vya kisheria ngazi ya Vijiji, Kata, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya na Kamati ya Ushauri ya Mkoa kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa tathmini ya vigezo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kwa sasa Serikali imeweka kipaumbele katika kuboresha na kukamilisha miundombinu msingi kwenye maeneo ya kiutawala yaliyopo ili yaweze kutoa huduma kwa ufanisi zaidi na baadaye kuendelea na maeneo mengine kwa kufuata taratibu na vigezo vilivyoainishwa, ahsante.
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. SEIF K. S. GULAMALI aliuliza: -

Je, lini Serikali itaugawa Mkoa wa Tabora na kupata Mkoa mpya wa Manonga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Seif Khamis Said Gulamali, Mbunge wa Jimbo la Manonga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mchakato wa kuanzisha eneo la Utawala la Mkoa unafanyika kwa mujibu wa sheria, kanuni na taratibu zilizopo baada ya Idhini/Kibali kutolewa na Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na kwa kuzingatia Sheria inayohusu kuanzisha Mkoa na Wilaya, Sura Na. 397 na Mwongozo wa kuanzisha Maeneo Mapya ya Utawala wa mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, maombi ya kuanzishwa Mkoa mpya yanatakiwa kujadiliwa, kupitishwa na kuridhiwa kwenye vikao vya Kisheria ngazi ya Vijiji, Kata, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya, Kamati ya Ushauri ya Mkoa kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa ajili ya tathmini ya vigezo.

Mheshimiwa Spika, kutokana na uhitaji mkubwa wa miundombinu na rasilimali nyingine katika mikoa iliyopo, Serikali imeweka kipaumbele katika kuboresha na kukamilisha miundombinu msingi kwenye maeneo ya kiutawala yaliyopo ili yaweze kutoa huduma kwa ufanisi zaidi na baadaye kuendelea na maeneo mengine kwa kufuata taratibu na vigezo vilivyoainishwa, ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Je, lini Serikali itatimiza ahadi ya kupeleka majokofu manne ya mochwari kwenye Kituo cha Afya Mugeta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa vifaatiba ikiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti katika vituo vya huduma za afya. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali ilitenga na kupeleka shilingi milioni 700 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa Halmashauri ya Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya fedha hizo, kiasi cha shilingi milioni 32.7 kimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa jokofu moja la milango sita la Kituo cha Afya cha Mugeta. Taratibu za manunuzi zinafanyika kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD) na inatarajiwa kukamilika kati ya mwezi huu Februari na Machi 2024. Ahsante.
MHE. BONIPHACE M. GETERE aliuliza:-

Je, lini Serikali itatimiza ahadi ya kupeleka majokofu manne ya mochwari kwenye Kituo cha Afya Mugeta?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Jimbo la Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuboresha upatikanaji wa vifaatiba ikiwemo majokofu ya kuhifadhia maiti katika vituo vya huduma za afya. Katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali ilitenga na kupeleka shilingi milioni 700 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba kwa Halmashauri ya Bunda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya fedha hizo, kiasi cha shilingi milioni 32.7 kimetengwa kwa ajili ya ununuzi wa jokofu moja la milango sita la Kituo cha Afya cha Mugeta. Taratibu za manunuzi zinafanyika kupitia Bohari Kuu ya Dawa (MSD) na inatarajiwa kukamilika kati ya mwezi huu Februari na Machi 2024. Ahsante.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA K.n.y. MHE. NORAH W. MZERU aliuliza:-

Je, lini Serikali itamalizia ujenzi wa zahanati ya Uwanja wa Ndege katika Kata ya Mafisa Mkoani Morogoro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Norah Waziri Mzeru, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kusogeza huduma za afya kwa wananchi wa Uwanja wa Ndege, mwaka wa fedha 2017/2018, Serikali ilipeleka shilingi milioni 70 kwa ajili ya ujenzi wa Zahanati ya Uwanja wa Ndege iliyopo katika Kata ya Kiwanja cha Ndege Manispaa ya Morogoro. Ujenzi umekamilika na huduma zimeanza kutolewa mwezi Mei, mwaka 2022. Zahanati hii kwa wastani huhudumia wagonjwa wapatao 750 kwa mwezi na wagonjwa 9,000 kwa mwaka, ahsante.
MHE. HAMISI S. TALETALE aliuliza: -

Je, lini Serikali itakamilisha Ujenzi wa Kituo cha Afya Kata ya Ngerengere?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hamisi Shabani Taletale, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kituo cha Afya Ngerengere kilisajiliwa mwezi Mei, 1995 na kinatoa huduma ya ngazi ya Kituo cha Afya ikiwa ni pamoja na huduma za upasuaji wa dharura na huduma nyingine. Aidha, kituo hiki kinahudumia wastani wa wagonjwa 1,200 kwa mwezi na 14,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kituo hiki kina upungufu wa baadhi ya miundombinu ikiwemo jengo la Huduma za Mama na Mtoto na Upasuaji, jengo la Maabara, jengo la kuhifadhia maiti na jengo la kufulia. Eneo la Kituo hicho lina ukubwa wa ekari nne na nusu, hivyo halitoshelezi mahitaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri ya Wilaya ya Morogoro, inaendelea kufanya mazungumzo na Shirika la Posta ambalo linamiliki eneo mkabala lenye ukubwa wa ekari mbili ambalo halijaendelezwa ili litumike kupanua Kituo cha Afya cha Ngerengere, ahsante.
MHE. CHARLES J. MWIJAGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Fibre Speed Boat mbili zilizofunikwa kama ambulance ili kusaidia Wananchi wa Visiwa 39 vya Wilaya ya Muleba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mhe Charles John Mwijage, Mbunge wa Jimbo la Muleba kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa kushirikiana na Wizara ya Afya imeandaa mpango mkakati utakaowezesha maeneo magumu kufikika kama visiwani na maeneo mengine kupata huduma za usafiri wa dharura pindi utakapohitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huo umeainisha vifaa vya usafiri vitakavyotumika kusafirisha wagonjwa ikiwemo usafiri wa anga yaani air ambulance na usafiri wa maji yani boat ambulance. Aidha, Mpango huo unatarajiwa kukamilika Disemba 2023 na kuanza utekelezaji katika mwaka wa fedha 2024/2025 na Wilaya ya Muleba itapewa kipaumbele, ahsante.
MHE. BENAYA L. KAPINGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itagawa Kata za Matiri, Litumbandyosi, Linda, Mkumbi, Litembo, Nyoni, Maguu na Langiro Wilayani Mbinga?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Benaya Liuka Kapinga, Mbunge wa Jimbo la Mbinga Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa kuanzisha maeneo mapya ya utawala upo kwa mujibu wa sheria za Serikali za Mitaa Sura ya 287 na 288 pamoja na mwongozo wa uanzishwaji wa maeneo ya utawala wa mwaka 2014, Hivyo Halmashauri ya Wilaya ya Mbinga inashauriwa kuanzisha mchakato wa maombi ya Kata za Matiri, Litumbandyosi, Linda, Mkumbi, Litembo, Nyoni, Maguu na Langiro kwa kufuata utaratibu ulioainishwa kwa kuanza na vikao vya ngazi za vijiji, Baraza la Madiwani, Kamati ya Ushauri ya Wilaya (DCC) na Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC) kisha kuwasilishwa Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kwa tathimini ya vigezo.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, kwa sasa Serikali imetoa kipaumbele katika kuboresha na kukamilisha miundombinu msingi kwenye maeneo yakiutawala yaliyopo ili yaweze kutoa huduma kwa ufanisi zaidi na baadae kuendelea na maeneo mengine kwa kufuata taratibu na vigezo vilivyoainishwa, ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali italeta Sheria ya kuruhusu halmashauri kutumia benki kama wakala wa ukopeshaji na ukusanyaji madeni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Yahya Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua ufanisi wa kutumia benki kama wakala wa ukopeshaji na ukusanyaji wa mmadeni kwa kuzingatia kuwa benki zina miundombinu na utaalamu wa kutoa huduma hizo. Hata hivyo, ili kutumia benki katika kutekeleza jukumu la mikopo ya asilimia 10, maandalizi na utafiti unapaswa kufanyika ili kuendana na lengo kusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, iliunda Kamati ya Kitaifa ambayo ilichambua na kuandaa mapendekezo ya uendeshaji wa mikopo inayotokana na asilimia 10 ya mapato ya ndani ya halmashauri. Aidha, timu imeshakamilisha kazi hiyo na kuwasilisha maoni na mapendekezo ambapo Serikali inaendeleia kuifanyia kazi na baada ya kukamilisha itatoa utaratibu, ahsante.
MHE. TECLA M. UNGELE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuzipatia magari ya wagonjwa Hospitali za Wilaya za Liwale, Nachingwea na Kilwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tecla Mohamed Ungele, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika mwaka wa fedha 2021/2022 kupitia Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano Dhidi ya UVIKO-19 itanunua magari 195 ya kubebea wagonjwa ambayo yatapelekwa kwenye halmashauri 184 nchini kote zikiwemo Halmashauri za Wilaya za Liwale, Nachingwea na Kilwa. Asante.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga kingo za Mto Kanoni unaopita katikati ya Mji wa Bukoba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Halmashaurii ya Manispaa ya Bukoba mwezi Februari, 2022 ilitumia shilingi milioni sita kupitia mapato ya ndani kwa ajili ya kusafisha, kupanua na kuongeza kina cha Mto Kanoni.

Mheshimiwa Spika, ili kuondoa changamoto hiyo Serikali katika mwaka wa fedha 2022/2023 imejumuisha mradi wa ujenzi wa kingo za Mto Kanoni kwenye Mpango wa TACTIC Awamu ya Pili unaotarajiwa kuanza mwezi Januari, 2023, ahsante.
MHE. NASHON W. BIDYANGUZE aliuliza:-

Je, lini Serikali itakamilisha ahadi ya shilingi milioni 10 za ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kazuramimba?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nashon William Bidyanguze, Mbunge wa Jimbo la Kigoma Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kutenga fedha kwa awamu kwa ajili ya ujenzi wa miundombinu katika Kituo cha Afya Kazuramimba. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali kupitia mapato ya ndani ya halmashauri ilitenga shilingi millioni 158 na kuendeleza ujenzi wa Jengo la wagonjwa wa nje (OPD) ambalo ujenzi wake upo katika hatua za ukamilishaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutenga fedha kupitia vyanzo mbalimbali na kuhakikisha inajenga na kukamilisha vituo vya afya kwenye maeneo ya kimkakati kote Nchini kikiwemo kituo cha Afya Kazuramimba, ahsante.