Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Condester Michael Sichalwe (1 total)

MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa hii nafasi, naomba kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, ipo tabia ambayo imezoeleka na sasa hivi imeota mizizi ndani ya Jimbo la Momba ambapo watu wanawakata watu mapanga kutokana na imani za kishirikina pamoja na baadhi ya migogoro ya ardhi. Katika kipindi cha miezi mitatu ambayo tulikaa hapa Bungeni kwenye Bunge la Bajeti zaidi ya watu watano waliuliwa; na siku nne zilizopita Diwani Mstaafu wa Kata ya Kapele ameuliwa kwa kitendo hicho hicho:-

Mheshimiwa Spika, ni nini tamko la Serikali ili kutusaidia kudhibiti tabia hii, ikiwezekana kuiondoa kabisa ili wananchi wa Jimbo la Momba tuweze kuishi kwa amani, upendo na mshikamano ili tuweze kujenga nchi? Ahsante sana. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Condester, Mbunge wa Momba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunayo migogoro ya jamii zetu kwenye ardhi kati ya jamii moja na nyingine, tuna migogoro ya jamii hasa walio kwenye mipaka ya hifadhi zetu, kati ya wahifadhi na wananchi, na pia kuna hiyo migogoro ya imani za kishirikina ambayo ipo sana katika jamii mbalimbali. Sasa sisi kama Serikali moja ni kusimamia; kwanza kutoa wito kwa Watanzania kuhakikisha kwamba nchi hii inabaki kuwa ya amani na utulivu na kwamba kila mmoja lazima azingatie sheria na kuzuia sana watu kuchukua hatua au sheria mkononi na kufanya mauaji.

Mheshimiwa Spika, sisi bado tunasimamia sheria. Pale ambapo linajitokeza tatizo la namna hiyo na mtu ameamua kuchukua sheria mkononi, naye tunamtia hatiani. Bado kutumia viongozi tuliowaweka kwenye maeneo hayo; Watendaji wa Vijiji kwenye ngazi ya Vijiji, Watendaji wa Kata kwenye ngazi ya Halmashauri na Wakuu wa Wilaya. Mkuu wa Wilaya ndio Mwenyekiti wa Kamati ya Ugawaji Ardhi kwenye Wilaya ile na anashirikiana na Halmashauri. Wao wameendelea kuelimisha jamii umuhimu wa kila mmoja kuzingatia sheria pale anapohitaji ardhi. Hata kama pale una ardhi halafu mwingine anaingilia, ni lazima ufuate mkondo katika kutatua migogoro.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nini Serikali inakifanya sasa? Kwanza kusimamia sheria ambazo zinagusa maeneo yote ikiwemo ya ulinzi na usalama, kuhakikisha kwamba hakuna mtu anachukua hatua kwa maamuzi yake; na kama itatokea tatizo, basi hatua thabiti ya kupeleka kwenye vyombo vya sheria, hiyo lazima izingatiwe.

Mheshimiwa Spika, pili, tunaendelea kufanya marekebisho kadhaa ya migogoro hii ya ardhi kati ya mtu mmoja na mwingine, kati ya jamii na maeneo haya ambayo yamehifadhiwa ili kufanya jamii inayozunguka maeneo hayo, jamii ambazo zinashirikiana katika kufanya kazi zao kila siku ziweze kuishi kwa amani. Hatua hii ndiyo inasaidia maeneo mengi sasa hivi kuwa tulivu na migogoro yote imeendelea kuratibiwa kwa kuunda Mabaraza ya Ardhi kwenye ngazi za Wilaya, Mikoa ili pale unapopata tatizo, kila mmoja aende kwenye chombo cha sheria. Hiyo ndiyo njia sahihi ya kuondoa migogoro hii.

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo utaratibu ambao kwa sasa tunausimamia kwa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu ili kufanya eneo hili kuwa la utulivu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)