Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Dr. Alfred James Kimea (12 total)

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya maji ya Busanda inafanana kabisa na changamoto ya maji iliyoko Korogwe Mjini. Nimekuwa nikifuatilia kwa Mheshimiwa Waziri na ameniahidi tatizo la Korogwe litatatuliwa na mradi wa miji 28 ambao Korogwe ni sehemu ya mradi huo.

Je, Serikali inawaahidi vipi wananchi wa Korogwe kwamba lini mradi huu utatekelezwa ili kuweza kutatua changamoto ya maji ambayo inawakabili wananchi wa Korogwe Mjini?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alfred Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nipende kumpongeza sana Mheshimiwa Mbunge kwa sababu amekuwa ni mfuatiliaji mzuri na nimeshaweza kuongea naye mara kadhaa na kumhakikishia eneo lake kupata maji na uzuri Korogwe Mjini ipo ndani ya ile miji 28 ambayo fedha tayari zipo na muendelezo wa maandalizi unaendelea na hivi karibuni kuanzia mwezi Aprili miji ile 28 shughuli za kupeleka maji zinakwenda kuanza mara moja.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nashukuru kwa majibu mazuri na Naibu Waziri, pia tunashukuru kwa ajili ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya matengenezo madogomadogo lakini matengenezo haya madogomadogo hayakidhi haja ya barabara hii kwani wakati wa mvua inaharibika kabisa na tunakosa mawasiliano kati ya mji mmoja hadi mwingine. Je, Serikali haioni kuna haja ya kutupa commitment ni wakati gani barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ili tutatue changamoto hii kabisa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alfred James Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara zote za changarawe ama za udongo na hasa maeneo ya mwinuko inaponyesha mvua huwa zinakuwa na changamoto ya kuondoka udongo ama changarawe. Commitment ya Serikali pamoja kutekeleza ahadi ya Rais na Waziri Mkuu tayari Serikali inatafuta fedha ili tuweze kufanya usanifu wa kina ili barabara hii iweze kujengwa kwa kiwango cha lami. Kwa hiyo, Serikali inatafuta fedha na fedha ikipatikana barabara hii itajengwa kwa kiwango cha lami. Ahsante.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona nami niulize swali dogo la nyongeza. Napenda kuipongeza Serikali kwani ndani ya Kata zangu zote 11 kwenye Jimbo la Korogwe Mjini umeme umefika, lakini changamoto ni kwamba ndani ya Kata hizo ipo Mitaa mingi ambayo umeme haujafika kabisa. Je, Serikali inawaahidi nini wananchi wa Korogwe katika kutatua changamoto hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, TANESCO inapeleka umeme katika maeneo mbalimbali kwa program za kila siku za kawaida, kwenye Mitaa, Vijiji na Vitongoji. Pia zipo program nyingine ambazo zinapeleka umeme kwenye Mitaa na Vijiji vyetu ikiwemo REA yenyewe, densification na peri-urban.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mheshimiwa Dkt. Alfred ambapo tayari Kata zake zote na vijiji vyake vyote vina umeme, yale maeneo machache ambayo hayana umeme, mradi wetu wa densification utapelekea umeme katika maeneo hayo kuanzia mwezi Saba. Pia tunavyo Vitongoji na Mitaa takribani kama 3,000 ambavyo vitapelekewa umeme, kwa hiyo, Vitongoji vyake na Mitaa yake Mheshimiwa Mbunge pia ni sehemu ya maeneo hayo yatakayopelekewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pale ambao densification tu itaanza mwezi wa Saba, Mheshimiwa ataweza kupata umeme katika eneo lake kwa sababu amekuwa akifuatilia sana ofisini kwetu na ni mfuataliaji mzuri wa maendeleo ya wananchi. Kwa hiyo, nawapongeza wananchi kwa kupata Mbunge mfuatiliaji kama wa aina yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, Nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Tuna Barabara yetu ya Korogwe Mjini ambayo inatokea Old Korogwe, Kwamndolwa, Magoma, Mashewa, Bombo Mtoni mpaka Mabokweni, ambayo ni ahadi ya Marehemu Rais Magufuli, Mama Samia na Waziri Mkuu. Je, ni lini Serikali itatekeleza ujenzi wa barabara hiyo kwa kiwango cha lami ili kutimiza ahadi ya viongozi wetu wa kitaifa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara alizozitaja Mheshimiwa Mbunge wa Korogwe zipo kwenye ahadi ya Rais na zipo kwenye Ilani na ni kati ya barabara ambazo zinakamilisha kilomita 6,006 ambazo zimeahidiwa kujengwa katika kipindi hiki cha miaka mitano. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, kadri fedha itakapopatikana barabara hizi ikiwemo na hii zitajengwa kwa awamu. Ahsante.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri, lakini kwa sasa hivi hatuna Mahakama ya Wilaya na shughuli za Mahakama ya Wilaya zinafanyika kwenye Mahakama yetu mojawapo ya Mwanzo ambayo haikidhi mahitaji ya Mahakama ya Wilaya: Huoni kuna haja sasa ya Serikali kuharakisha ujenzi wa Mahakama yetu ya Wilaya ya Korogwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza shughuli za Mahakama ya Wilaya ambazo zilitakiwa zifanywe na Mahakama ya Wilaya katika Wilaya ya Korogwe, mwanzo zilikuwa zinafanyika katika ofisi ndogo sana ya Mkuu wa Wilaya ya Korogwe. Kwa sasa tumeweza kukarabati jengo ambalo tumepewa na Halmashauri ya Korogwe ambalo kimsingi linakidhi mahitaji ya Mahakama hiyo. Hivyo basi, kama tulivyokwishatoa maelezo ya msingi kwenye jibu la msingi kwamba, ifikapo kipindi kijacho cha fedha, tunakwenda kuanzisha ujenzi wa Mahakama ambayo sasa itakuwa ni ya Wilaya ya Korogwe. Ahsante.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, kimsingi hospitali yetu hii ni kongwe sana inawezekana ni kati ya hospitali kongwe zaidi Tanzania ambayo ilijengwa mwaka 1952.

Je, Serikali inatupa commitment gani kwamba tutapewa fedha hizi maana tumekuwa tukiahidiwa mara nyingi tunaletewa fedha za ukarabati na hatujawahi kupewa.

Je, Serikali ina tupa commitment gani kwamba fedha hizi zitakuja ili hospitali yetu hii ipate kukarabatiwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimetoa majibu yangu ya msingi katika mwaka wa fedha 2023/2024 hospitali hii kongwe ya Mjini Korogwe ya Magunga imeshatengewa shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii. Kwanza naipongeza na kuishukuru Serikali kwa kutupatia fedha kwa ajili ya bonde hili moja. Tunaiomba Serikali itupatie fedha kwa mwaka unaofuata kwa ajili ya Bonde la Kwamngumi pamoja na Bonde la Kwamsisi kwenye Halmashauri yetu ya Korogwe Mjini.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Dkt. Alfred James Kimea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumepokea maombi yake na kama nilivyosema katika majibu yangu ya msingi, tayari Kwamngumi tumeshaingiza katika Mpango wa mwaka 2023/2024 kwa ajili ya upembuzi yakinifu. Hivyo nimwondoe hofu, ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba inawekeza katika miundombinu ya umwagiliaji. Tutapitia tena na maeneo mengine ambayo ameyataja hasa katika eneo la Kwamsisi.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii; kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini tuna skimu kubwa mbili za umwagiliaji Bonde la Mahenge Nagoo lakini pamoja na Bonde la kwa Mngumi. Mwaka huu Serikali ilituahidi itatupatia shilingi milioni 600 kwa ajili ya ukarabati wa Bonde la Mahenge pamoja na Nagoo, lakini mpaka muda huu ninavyoongea hatujapata hata shilingi moja kwa ajili ya ukarabati huo.

Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Korogwe Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Alfred Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, sababu za kwa nini fedha hazijafika mpaka hivi sasa ni kwamba skimu hizo mbili alizozisema zinategemea sana Bonde la Bwawa Mkomazi. Kilichofanyika hivi sasa ni kwamba tumeamua tuanze na zoezi kubwa la upembuzi yakinifu na usanifu wa Bonde la Mkomazi kwanza ili baadaye tuweze kuzifikia hizo skimu mbili. Nimuondoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba tarehe za mwanzo kabisa za mwezi wa saba consultant atapatikana kwa ajili ya Bonde hilo la Mkomazi na baadaye kazi hiyo ikikamilika tutaendelea na hizo skimu mbili ambazo amezitaja kwa Mkumbo na ile nyingine. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kati ya changamoto kubwa zinazowapata wafanyabisahara wadogo hawa tunaowaita machinga ni uwezo wa kupata mikopo kwenye hizi financial institutions zetu, na sababu kubwa ni kutokidhi vigezo, hasa dhamana na wale wachache ambao wanapata mikopo haswa kwenye hizi micro-finance riba ni kubwa sana hivyo inasababisha wao kushindwa kuendeleza biashara zao.

Je, Wizara imejipanga namna gani ili kuweza kuwasaidia watu hawa kwenye sekta hii niliyoitaja? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Alfred Kimea, Mbunge wa Korogwe Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli, changamoto kubwa ambayo inawakumba wajasiriamali ikiwemo wamachinga ni changamoto ya kupata fedha au mitaji kwa ajili ya kufanya shughuli zao. Serikali inachukua jitihada mbalimbali ikiwemo kuweka fedha mahususi kwa ajili ya kuwasaidia wamachinga, kama ile asilimia 10 ya mikopo kupitia Halmashauri zetu, lakini pia zaidi kupitia taasisi zetu kama SIDO ambayo inahudumia viwanda vidogo na wafanyabiashara wadogo, tumeshaweka mahususi kwanza fedha, lakini pili tumekubaliana kupunguza ile riba ambayo mwanzoni ilikuwa ni kubwa kwa hiyo, itakuwa chini ya asilimia 10, lakini zaidi tunaendelea kuongea na taasisi za kifedha za binafsi na ninyi ni mashahidi, tarehe 11 Aprili Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, alifungua ile kampeni ya teleza kidijitali ambapo mfanyabiashara au mmachinga mdogo anaweza kupata fedha bila kuwa na dhamana au kwenda benki kupitia simu ya kiganjani, wanasema Mshiko Fasta kuanzia shilingi 50,000 mpaka 500,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii ni jitihada kuhakikisha tunamkomboa mfanyabiashara mdogo au mmachinga kupata fedha kirahisi zaidi. Nakushukuru.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii kuuliza swali la nyongeza. Pia napenda kuipongeza Serikali kwa majibu yake mazuri na yenye kutia matumaini kwa wananchi wa Kata ya Kwamsisi pamoja na Kwamngumi kwa kuwa hiki kilikuwa kilio chetu sisi sote.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza, ninahitaji commitment ya Serikali kwamba ni kweli mwaka huu tutaenda kujengewa Skimu hii ya Kwamsisi na mwakani tutaenda kujengewan Skimu ya Kwamngumi maana imekuwa ahadi ya siku nyingi. Kwa hiyo, naomba commitment ya Serikali kwamba jambo hili linaenda kutokea mwaka huu na mwaka ujao.
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kama ambavyo nimejibu katika jibu la msingi, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Korogwe Mjini, ahadi ya Serikali tulivyoahidi hapa itatekelezeka kwa asilimia mia moja. Hiki ninachokizungumza, nina uhakika nacho, ahsante sana. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mwaka 2021 Kata ya Mgombezi kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini walipatiwa shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya. Baadhi ya majengo yalijengwa lakini mpaka sasa tunapoongea, shilingi milioni 250 za ziada hazijafika kwenye ile Kata ya Mgombezi, zaidi ya miaka miwili. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, ni lini Serikali itatuletea shilingi milioni 250 zilizobaki ili kwenda kumalizia Kituo cha Afya cha Mgombezi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna Vituo vya Afya katika Majimbo mengi hapa nchini ambavyo vilipewa shilingi milioni 250 mwaka wa fedha 2021/2022 na majengo ya shilingi milioni 250 yamekamilika, yameanza huduma za awali za OPD kwenye baadhi ya Vituo lakini kuna majengo yanayohitajika kwa ajili ya kukamilisha ngazi ya Kituo cha Afya. Naomba kumhakikishie Mheshimiwa Kimea kwamba tunatambua Vituo vyote ambavyo vimepata shilingi milioni 250 na bado shilingi milioni 250.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametupa kibali kuweka kwenye bajeti ambayo tunaanza kuipanga hivi karibuni, kuhakikisha Vituo vyote vya Afya vilivyopata shilingi 250 na bado shilingi milioni 250, vinapelekewa mwaka ujao wa fedha ili vituo vile viweze kukamilika, ahsante. (Makofi)
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Mwaka 2021 Kata ya Mgombezi kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini walipatiwa shilingi milioni 250 kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Afya. Baadhi ya majengo yalijengwa lakini mpaka sasa tunapoongea, shilingi milioni 250 za ziada hazijafika kwenye ile Kata ya Mgombezi, zaidi ya miaka miwili. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Waziri, je, ni lini Serikali itatuletea shilingi milioni 250 zilizobaki ili kwenda kumalizia Kituo cha Afya cha Mgombezi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Kimea, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna Vituo vya Afya katika Majimbo mengi hapa nchini ambavyo vilipewa shilingi milioni 250 mwaka wa fedha 2021/2022 na majengo ya shilingi milioni 250 yamekamilika, yameanza huduma za awali za OPD kwenye baadhi ya Vituo lakini kuna majengo yanayohitajika kwa ajili ya kukamilisha ngazi ya Kituo cha Afya. Naomba kumhakikishie Mheshimiwa Kimea kwamba tunatambua Vituo vyote ambavyo vimepata shilingi milioni 250 na bado shilingi milioni 250.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametupa kibali kuweka kwenye bajeti ambayo tunaanza kuipanga hivi karibuni, kuhakikisha Vituo vyote vya Afya vilivyopata shilingi 250 na bado shilingi milioni 250, vinapelekewa mwaka ujao wa fedha ili vituo vile viweze kukamilika, ahsante. (Makofi)