Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Alfred James Kimea (10 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii uliyonipatia ili niweze kuchangia kwenye Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuongea mbele ya Bunge lako Tukufu, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii kuwa kati ya wawakilishi wa wananchi kwenye Bunge hili la Kumi na Mbili. Nafahamu umuhimu na ukubwa wa nafasi hii, hivyo, namuomba Mwenyezi Mungu akapate kunipa busara na hekima hasa kwa hiki kipindi changu cha miaka mitano ili niweze kuwaongoza watu wake kwa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepata fursa ya kuusoma vizuri Mpango huu lakini kutokana na muda nimeamua ushauri wangu wote wa kitaalam niuweke kwenye maandishi hivyo baada ya hapa nitakabidhi meza yao ushauri wangu huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa hizi dakika chache ulizonipatia, naomba niongee mambo machache hasa yanayohusiana na Jimbo langu la Korogwe Mjini. Nafahamu Mpango huu hasa umejikita kuimarisha uchumi kwenye Sekta ya Viwanda na Biashara. Hata hivyo, ili tuweze kufikia malengo hayo, naomba tuzingatie ushiriki wa wanawake katika uchumi wa viwanda na biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu umuhimu wa wanawake katika kukuza uchumi. Hii hata kwenye Biblia inadhihirishwa, inasema wanawake ni Jeshi kubwa. Hata hivyo, ushiriki wa wanawake kwenye sekta ya uchumi umeathiriwa sana na changamoto mbalimbali kwenye jamii zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini, ushiriki wa wanawake kwenye shughuli za uchumi na biashara pamoja na viwanda umeathiriwa sana na tatizo la maji. Wamama wa Korogwe badala ya kujihusisha kwenye shughuli za kiuchumi wamekuwa wakipoteza muda mwingi kutafuta maji kwa ajili ya kuhudumia familia zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maji yamekuwa changamoto kubwa ambayo imewapotezea focus wamama wa Korogwe hivyo kupunguza kasi ya uchumi na maendeleo ya Jimbo letu la Korogwe Mjini. Hivyo nimuombe kaka yangu Mheshimiwa Aweso aone namna gani tunatatua tatizo hili ili akina mama wa Korogwe wakape fursa ya kushiriki kwenye uchumi badala ya kuhudumia familia zao kutafuta maji usiku mzima. Kwa wastani kwenye Jimbo langu tunapata maji mara moja kwa wiki, hivyo tunaomba tuangaliwe kwa jicho la kipekee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu pasipo afya bora ni vigumu kuweza kufikia haya maendeleo tuliyoyaainisha kwenye Mpango huu. Hivyo, kwenye sekta ya afya kwenye Jimbo langu la Korogwe pia ni changamoto kubwa. Tuna hospitali yetu moja ya wilaya ambayo tunaitegemea kwenye Jimbo letu la Korogwe, lakini sio Korogwe tu pamoja na wilaya nyingine za jirani; hospitali hii ni chakavu sana imejengwa tangu mwaka 1952 hivyo haiwezi kukidhi mahitaji ya huduma za afya kwenye jimbo letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo naomba Wizara husika ione namna gani inatutatulia changamoto hii. Aidha, tukarabatiwe hospitali ile kwa viwango vikubwa au kujengewa hospitali nyingine, ili watu wapate afya bora tuweze kukimbizana na shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naomba niweze kuungana na watu wengine wengi waliochangia, umuhimu wa miundombinu ya barabara katika kukuza uchumi na kuweza kufikia Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini tuna barabara muhimu sana, barabara hiyo inatuunganisha watu wa Korogwe Mjini, watu wa Korogwe Vijijini, pamoja na Mkinga. Barabara ambayo inatokea Korogwe – Kwa Mndolwa – Magoma, tuliahidiwa na Rais pamoja na Waziri Mkuu tutatengenezewa barabara hii, hivyo namwomba Waziri mhusika wa Wizara hii aweze kutujengea barabara hiyo ili kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nichangie kwenye hii bajeti ya Wizara ya Elimu. Nina mambo machache sana ya kuchangia kwenye Wizara hii na napenda nijikite hasa kwenye elimu ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya changamoto ambazo zimetolewa imeonekana tuna upungufu wa Wakufunzi au Wahadhiri katika vyuo vyetu, lakini tuangalie ni nini kinasababisha kitu hiki? Kama tunafahamu vyuo vyetu vina tendency ya ku-retain wanafunzi waliofanya vizuri wabaki kufundisha wanafnzi wetu, lakini pia kufanya research ambazo zinasaidia kutatua changamoto zinazopatikana kwenye jamii zetu. Ili mwanafunzi awe retained pale chuoni ni lazima wawe ni wanafunzi wanaofanya vizuri, First Classes ndio zinabakizwa vyuoni. First Class hizi hazihitajiki chuoni tu peke yake, pia mashirika mbalimbali yanatafuta watu hawa. Kwa hiyo, maslahi ya wanaobakishwa pale chuoni ndio yanayosababisha aidha mwanafunzi huyo au wanafunzi hao wazuri wakubali kubaki chuoni au waende sehemu nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa niishauri Serikali, ione namna ya kuboresha maslahi kwa wataalam wetu hawa ambao wana kazi kubwa ya kufanya research, wana kazi kubwa ya kufundisha wanafunzi wetu vyuoni, ili waweze kuwa na morali ya kubaki vyuoni kuliko kwenda kuajiriwa sehemu nyingine. Huo ndio mchango wangu wa kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, naongea hili kwa kuwa nina uzoefu na nilikuwa miongoni mwa watu hao, labda kwanza naomba ku-declare interest. Nadhani unafahamu ugumu wa kupanda madaraja kwenye vyuo vyetu, tunaajiriwa mara nyingi kutoka vyuoni kama Tutorial Assistant, baada ya kupata Masters tunaenda kuwa Assistant Lecturer na baada ya hapo tunakuwa ma-lecturer aidha kwa ku-publish baada ya kukaa miaka mitatu au kupata Ph.D.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo,watu hawa wanaweza wa-qualify. Mtu amehangaika sana aka-publish au kapata Ph.D anapanda cheo kwa kuandikiwa tu barua umepanda, lakini wanasema tunasubiri Serikali itoe idhini ya kupandishwa vyeo ili mpewe maslahi yenu. Hii inakatisha moyo wakufunzi wetu, inasababisha watu waondoke vyuoni; tunasema Wahadhiri ni wachache, lakini Serikali ndio inasababisha. Kwa kweli, hii ni sehemu nyeti sana, tunaomba maslahi ya watu hao yaangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano ni wa kwangu mimi mwenyewe, kabla ya kwenda kufanya PhD nili-publish ili niweze kupanda kuwa Lecturer kabla ya kwenda PhD. Nilipewa tu barua ya pongezi kwamba, nime-qualify kuwa Lecturer, lakini hadi leo sijawahi kupata mshahara wa mtu kama Lecturer. Kwa hiyo, nasema wapo wenzangu wengi huko vyuoni wana changamoto kama ya kwangu, naomba tuangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine, tunajua mazingira ya kusoma hapa Tanzania. Najua unaweza kuwa unafahamu watu ambao wamefanya Ph.D zao hapa Tanzania, kuna changamoto kubwa, lakini changamoto hii inasababishwa na maslahi mabovu ya wasimamizi wa Ph.D zile. Lecturer hana kipato kizuri, inasababisha aanze kutafuta shughuli nyingine za kumuingizia kipato. Utakuta lecturer anafundisha part time vyuo vinne, utakuta lecturer anafuga kuku ili kujiongezea kipato, anaacha kusimamia dissertation za wanafunzi. Kwa hiyo, kama tunataka kupandisha elimu ya vyuo vyetu, basi tuangalie maslahi ya watu hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sio hilo tu, pia vyuo vyetu havina fund kwa ajili ya kuendesha research. Sio research tu, ili uweze kutoa watu wa masters na PhD lazima vyuo viwe vime-subscribe kwenye journal nzuri za kimataifa, viwe vina software kwa ajili ya data analysis, lakini vyuo havipatiwi fedha hizi. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ivipatie fedha vyuo vyetu ili elimu iweze kukua, hasa research ambazo zinahitajika kwa ajili ya maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, cha mwisho, naomba Wizara ya Elimu inisikilize kwa makini; kulikuwa kuna institute hapa Tanzania inaitwa African Institute for Mathematical Science. Institute hii ipo South Afrika, Ghana, Tanzania na Rwanda, lakini institute hii inafadhiliwa na wafadhili (Donors) kwa asilimia kubwa na nchi ambayo hii institute ipo nchi hiyo inatoa kiasi kidogo kwa ajili ya uendeshaji wa chuo hicho, lakini Serikali yetu imeshindwa kulipia fedha kidogo kwa ajili ya kuendesha institute hiyo na institute hiyo imekufa. Namwomba Waziri kwenye majumuisho yake aje aniambie kimetokea kitu gani kwa institute hii mpaka kufa?

Mheshimiwa Naibu Spika, institute hii inasaidia researcher wetu, institute hii inasaidia wataalam wetu kuweza kufundishwa jinsi ya ku-apply mathematics kwenye kutatua matatizo kwenye jamii zetu. Imefanya vizuri sana Rwanda na inaendelea kufanya vizuri, imefanya vizuri Ghana na inaendelea kufanya vizuri, Tanzania kuna nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Huo ndio ulikuwa mchango wangu. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, lakini napenda tuweke taarifa sahihi, jina langu ni Alfred Kimea na sio Kimei.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa hii nafasi, wenzangu wameongea mengi. Ukianza kufuatilia utaona kila mchango ambao unatakiwa kwenda kwa Wizara hii kwenye hii Bajeti Kuu ya Serikali, imeshaongelewa. Napenda tu niongezee machache na sehemu nyingine niongezee ambapo palishaongelewa kwa sababu mengi yameshaongelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza napenda kumshukuru Rais wetu Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya. Tusiposhukuru kwa kazi kubwa anayoifanya, tutakuwa hatumtendei haki mama huyu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kipindi kichache tangu tuwepo Bungeni mambo makubwa, aidha yameshafanyika au tumepewa ahadi kubwa kwa ajili ya kuendeleza majimbo yetu. Mfano tu kwenye jimbo langu la Korogwe Mjini, kwa kipindi hiki kidogo tumeshaandaliwa zaidi ya shilingi bilioni mbili kwa ajili ya sekta ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu ni la Korogwe Mjini, kwa kipindi hiki kidogo tumekwisha kuandaliwa zaidi ya bilioni mbili kwa ajili ya sekta ya maji. Sekta ya barabara ikiwemo TARURA tuna bajeti ya karibu 1,300,000,000 kwa hiyo, hii ni kitu kikubwa ni lazima tumshukuru Mama kwa kazi kubwa anayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikija kwenye bajeti sasa, mchango wangu utakuwa wa sehemu mbili, moja nitapongeza lakini sehemu ya pili nitashauri sehemu chache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa pongezi kwa kweli tunamshukuru na tunampongeza kweli Waziri, wetu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu pamoja na kaka Mheshimiwa Engineer Masauni kwa kazi kubwa waliyoifanya kwa kutuletea hii bajeti nzuri. Kwa kweli ni bajeti nzuri ambayo inatakiwa kupongezwa na ninazo sababu ya kupongeza hii bajeti siyo tu kama nafuata mkumbo wa watu wameipongeza bajeti na mimi nipongeze lakini ninazo sababu kabisa za msingi kwa ajili gani naipongeza hii bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha kwanza ni kweli hii bajeti imekwenda kumgusa kila mtanzania. Kila Mtanzania ameguswa kwenye hii bajeti kuanzia wafanyakazi tumeona wanakwenda kupandishwa vyeo na hii tuliipigia kelele sana mimi nilikuwa mmoja wapo nilisema walimu hasa wa vyeo vikuu ambao mimi nilitoka huko nilikuwa mmoja wao walikuwa wanastahili kupandishwa madaraja lakini kwa muda mrefu hawakuwa wanapandishwa madaraja. Lakini hii bajeti sasa imekuja na dawa hiyo; walimu wa Vyuo Vikuu wanakwenda kupandishwa madaraja. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kwa ajili ya kuona hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia bajeti hii imegusa au imezingatia maoni ya Wabunge na Wadau wengine wengi. Hajakaa tu chini kuandaa bajeti, hajachukua template za bajeti zilizopita, amekaa chini kuangalia Wabunge waliongea kitu gani, alikaa chini kuangaliwa wadau wanazungumza kitu gani akaja na bajeti nzuri ambayo imezingatia maoni ya watu hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulishauri juu ya TARURA kuongezewa bajeti na kweli TARURA imekwenda kuongezewa bajeti. Tulishauri Wizara ya Afya iongezewe bajeti na wamefanya hivyo. Tulishauri miradi mikubwa iende kufanyika na kweli wanakwenda kuiendeleza ile miradi mikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ndugu yangu Mheshimiwa Waziri kwa kuwa umesema unakwenda kufanya vitu hivyo, kweli tunataka hivyo vitu vikafanyike. Mfano mmojawapo; tunakwenda kushika kodi kwenye line za simu na tunakwenda kuchukua kodi kwenye mafuta na alisema specific kwenye mafuta shilingi 100 inakwenda TATURA na kwenye line inakwenda kwenye huduma za afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania siyo watu wajinga, wanakwenda kuhesabu kitu gani kinakwenda kupatikana na kitu gani kinakwenda kufanyika. Kwa kuwa ulisema specifically hii inakwenda kwenye afya kweli tunataka iende kwenye afya. Tumesema hii inakwenda TARURA kweli tunataka hii iende TARURA. Kwa hiyo, tunakupongeza lakini tunataka kweli ahadi yako uende kuitimiza kwa ajili tuna mwaka mmoja tu, mwakani siku kama hizi tutarudi tena tukikupitishia bajeti nyingine tunataona hiki kitu umekifanya kwa namna gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sehemu nyingine ya mwisho, kwa ajili gani naipongeza hii bajeti kama kauli mbiu ya nchi yetu ni kuinua uchumi wa viwanda ni kweli bajeti hii imeonesha dhamira yake ya kwenda kuinua uchumi wa viwanda. Tumeona wakipunguza baadhi ya ushuru wa forodha kwa bidhaa ambazo zinakwenda kutumika kwenye viwanda vyetu. Lakini pia wameongeza ushuru wa forodha kwenye bidhaa ambazo zinatengenezwa Tanzania ili kuweza kuinua sekta ya viwanda kwenye nchi yetu. Kwa hiyo, tunaipongeza bejeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema mchango wangu utakuwa na sehemu mbili. Sehemu ya kwanza ni pongezi ambayo nimekwisha kutoa lakini sehemu ya pili ni maoni yangu kwenye baadhi ya maeneo machache ambayo naona yanahitaji kufanyiwa marekebisho. Ya kwanza, nitoe maoni yangu kwenye hii sheria ya kodi ya majengo. Kweli Mheshimiwa Waziri nakupongeza kwa hii kodi mpya au namna ya utozaji wa hii kodi mpya. Kama tunavyofahamu ni kweli kodi yoyote ambayo inaanzishwa ni lazima iwe nyepesi kukusanya. Kweli nakupongeza hii kodi ambayo umeianzisha itakwenda kuwa rahidi kukusanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kodi mpya inayoanzishwa ni lazima iwe na urahisi wa kulipa. Ni kweli walipo kodi wetu itakuwa rahisi kuilipia hii kodi ya majengo kuliko mwanzo ilivyokuwa. Lakini kuna principle nyingine ya kodi inaitwa principle diversity kwamba mtu yoyote ambaye anakusudia kulipa hii kodi kweli anatakiwa kulipa hiyo kodi na kweli kodi hii itakuwa vigumu sana kwa mtu yoyote ambaye kakusudia kulipa kukwepa kodi hii. Kwa hiyo napongeza kwa jitihada hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti kodi hii inachangamoto kidogo ambazo kidogo ambazo lazima Mheshimiwa Waziri waweze kuzi-address. Ya kwanza tunafahamu kodi yoyote kuna principle muhimu sana ambayo hii kodi inakwenda kinyume na principle hiyo. Principle ya Equity, kwamba watu wenye kipato sawa waweze kulipa kodi sawa; lakini watu wenye vipato tofauti basi kodi iwe tofauti, mwenye kipato kikubwa alipe kodi kubwa na mwenye kipato kidogo alipe kodi ndogo. Lakini Mheshimiwa Waziri utakubaliana na mimi kabisa kwamba kodi jinsi ilivyo wewe Mheshimiwa Waziri utakwenda kulipa shilingi 1,000 kwa mwezi, na yule bibi yetu kule nyumbani kwetu kwa Mndolwa, kule nyumbani kwetu Old Korogwe naye atakwenda kulipa sawasawa na wewe ulivyolipa. Hii siyo sawa kabisa Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, lazima hii kodi ije itengenezwe namna kwamba mwenye kipato kikubwa atalipa kodi kubwa na mwenye kipato kidogo atalipa kodi ndogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, madhara ya hiki, moja itawadhulumu wale watu wanyonge; lakini namba mbili Serikali haitakusanya mapato yake sahihi kwa ajili mtu mwenye kipato kikubwa atalipa sawa na yule mwenye kipato kidogo. Nini kifanyike; maoni yangu, nadhani haya yataondoa ile shida ambayo Wabunge wengi wameiongea. Maoni yangu ni kwamba kwanza assumption zangu ni kwamba mtu ambaye anatumia unit nyingi atakuwa na kipato kikubwa kuliko mtu anayetumia unit ndogo. Sasa kwa namna gani mtu mwenye kipato kidogo atalipa kidogo na mwenye kipato kikubwa atalipa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, badala ya kusema unashika kodi shilingi 1,000 kwenye Luku achana na hiyo, shika kutokana na matumizi ya Unit, badala ya Luku shika hiyo kodi kwenye unit mtu anazotumia. Ukifanya hivyo Mheshimiwa Waziri; moja mtu mwenye kipato kidogo atalipa stahiki yake, mwenye kipato kikubwa atalipa stahiki yake. Namba mbili, ile issue ya maghorofa mtu ana ghorofa ngapi? Mtu ana apartment ngani, hiyo hutaizingatia tena kwa ajili mtu mwenye kikubwa atatumia sana na alipa kodi kubwa na mtu mwenye kanyumba kadogo atalipa kidogo. Kwa hiyo nashauri badala ya kukatwa hiyo kodi kwenye mita ikatwe kwa Unit jinsi mtu anavyotumia. Huo ndio ushauri wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kodi nyingine ambayo napenda kushauri kidogo ni tozo kwenye line za simu. Kengele ya kwanza naamini. Tozo kwenye line ya simu. Mheshimiwa Waziri, hapa tozo kwenye line ya simu lazima uwe clear hii kodi inakwenda kushikwa kwenye nini; kwa ajili kila kodi mpya inayoanzishwa lazima tujue base ya hiyo kodi ni kitu gani? Aidha, unakwenda kushika kodi kwenye line ambayo siamini kwamba umiliki wa line unaweza kumshika mtu kodi au unakwenda kushika kodi kwenye matumizi ya muda wa maongezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama ni kwenye matumizi muda wa maongezi ile item uliyoisema kwa siku itakuwa siyo muhimu. Kama unakwenda shika hii kodi kwenye muda wa maongezi kuna mtu anaweza akaongeza muda wa maongezi mara kwa wiki, mwingine akawa anamiliki line tu lakini haongezi muda wa maongezi. Kwa hiyo ukisema unamshika ile kodi kila siku hutakuwa umemtendea haki. Kwa hiyo, naamini watakaoshika hii kodi per muda wa maongezi na pia inatakiwa um-charge mtu kwa jinsi anavyoongeza muda wa maongezi. Kwa hiyo, hayo ndio maoni yangu, naomba kodi hizo zifanyiwe kazi ili kodi zetu ziweze kuleta tija zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha mwisho kama muda upo, naomba nishauri kwenye ushuru wa forodha kwenye mafuta. Kweli Mheshimiwa Waziri naamini kabisa kodi hii ni kwa ajili ya kulinda viwanda vyetu lakini sasa hivi Tanzania bado tuna deficit ya mafuta. Kwa hiyo, kodi ni nzuri lakini ninachoona timing bado. Tuhimize watu wetu wazalishe mbegu za alizeti pale tutakapokuwa tuna-produce zaidi hapo ndio tuanze ku-protect hatuwezi kuanza ku-protect kitu ambacho hatunacho bado. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kodi hii ni nzuri na ninaiunga mkono lakini nahisi timing bado sasa hivi mahitaji ya nchi yetu ni karibu tani za ujazo 500,000, zaidi ya 500,000 lakini tuna produce 200,000 tu. Kwa hiyo, tukienda ku-protect sasa hivi kitu ambacho hakipo bado haiingia akilini kwa hiyo naomba tuwahimize watu wetu na tutakapokuwa tunazalisha zaidi hapo ndipo tutakapokuwa na nafasi ya kuweza kulinda viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa muda huu, naunga mkono hoja, mungu awabariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Elimu. Kwanza niwapongeze viongozi wa Wizara hii ya Elimu. Kwanza Ndugu yangu Mheshimiwa Profesa Mkenda, kaka yangu Mheshimiwa Omari Kipanga, Katibu Mkuu Profesa Nombo pamoja na Manaibu Katibu Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya kuhakikisha wanasimamia sekta hii ya elimu kwenye nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, napenda kuishukuru Serikali ya Tanzania ambayo inaongozwa na Rais wetu, Jemadari kabisa, mama jembe, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kunyanyua sekta ya elimu kwenye nchi yetu. Mambo mengi yamefanyika, lakini nitazungumzia machache wala siwezi kuyaongea yote yaliyofanywa kwenye sekta ya elimu hasa kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini. Yamefanywa mambo mengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia vyoo, wanafunzi walikuwa wanapata shida lakini tumejengewa vyoo kwenye kila shule ya sekondari na shule ya msingi. Ukizungumzia maabara, kwenye shule zote za sekondari tumejengewa, ukizungumzia mabweni na miundombinu mingi kwenye sekta ya elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, vitu vikubwa ambavyo nataka kuvitaja wananchi wa Korogwe ambao wanatamani kuvisikia Mama Samia amevifanya; moja, katujengea sekondari mpya kabisa kwenye Kata ya Bagamoyo na sasa hivi sekondari nyingine inaendelea kujengwa kwenye Kata ya Mtonga kwenye Kijiji cha Msambiazi. Hayo ni mambo makubwa, lakini hivi tunavyoongea, tayari tumeletewa fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule mpya ya msingi na mambo mengine mengi yanafanyika kwenye sekta ya elimu. Kwa hiyo, hatuna budi kumshukuru na kumpongeza mama yetu, jembe kabisa, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaifanya. Kimsingi, baada ya miaka yake 10 ya uongozi, ataacha historia kubwa kwenye nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo, pia nitumie fursa hii kwa ufupi kabisa kuwapongeza viongozi wangu wa Halmashauri ya Korogwe Mji, hasa viongozi kwenye sekta ya elimu, nikizungumzia Afisa Elimu, Walimu pamoja na wadau wengine wa elimu kwenye Jimbo langu la Korogwe Mji. Kwenye Halmashauri yetu tunaongoza kwenye ubora wa elimu kwenye Mkoa wa Tanga. Hivyo, nawapongeza lakini nataka niwatie moyo waendelee kufanya kazi kwa juhudi, tuko pamoja nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuongea hayo, shukurani na pongezi hizi huwa zina tafsiri yake kwa nyuma kwamba bado tunahitaji vitu vingine. Tunajua vingi vimefanywa lakini bado tuna changamoto chache kwenye shule zetu. Bado tuna upungufu wa baadhi ya madarasa, vyoo na shule nyingine ni chakavu, lakini naamini kabisa kwa kasi hii ya Rais wetu, tutaletewa hivyo vitu na baada ya miaka yetu mitano ya uongozi na Mama Samia akiwa madarakani mambo mengi yatafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa hilo. Hiyo ilikuwa sehemu yangu ya kwanza ya mchango wangu. Sehemu ya pili ni hoja yangu ya msingi kwenye siku ya leo, namwomba Mheshimiwa Prof. Mkenda apate kunisikiliza kwa umakini ili kama Taifa tuweze kufanya maamuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo asubuihi alisimama ndugu yangu Mheshimiwa Maige kuzungumzia lugha ya kufundishwa kwenye shule zetu, lakini muda mchache amesimama ndugu yangu Mheshimiwa Erick Shigongo, nami pia nilikuwa na mchango kama huo huo. Sipingi kwamba lugha ya Kiswahili ni lugha yetu ya Taifa. Tunaipenda, tunajivunia lugha hii na kila mtu, sio mimi tu, nadhani kila Mtanzania anatamani lugha hii ikapate kuzungumzwa East Africa yote, ikapate kuzungumzwa Afrika nzima na hata dunia nzima. Ni lugha yetu, tunaipenda, nitaendelea kuipenda siku zote. Isipokuwa, sisi kama Taifa hatupaswi hata kidogo kupuuzia mchango wa lugha ya Kiingereza kwenye dunia hii na kwenye mchango wa uchumi wa nchi yetu. Sisi kama Taifa hatupaswi kupuuzia hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaeleza kwa uchache faida za lugha ta Kiingereza. Moja, nitaeleza faida kwa mtu binafsi, halafu baadaye nitaeleza faida kama Taifa. Kwenye dunia hii, watafiti wanasema, mtu mwenye uwezo mzuri wa kuweza kuongea vizuri lugha ya Kiingereza, akaweza kuiandika na kuisikia vizuri ana chance kubwa ya kuajirika kuliko mtu mwingine yeyote. Huo ndio utafiti unasema hivyo. Sisi kama Taifa hatutakiwi kupuuzia utafiti huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia utaungana nami, kwenye nchi yetu, interview karibu zote zinafanyika kwenye lugha ya Kiingereza. Kwa hiyo, sisi kama Taifa pia tunafahamu umuhimu wa lugha ya Kiingereza. Pamoja na hilo, ili uajiriwe kwenye makampuni makubwa kwenye dunia hii, nenda Google, nenda Facebook, nenda Spacex na makampuni mengine yote, ni lazima uwe na uwezo mkubwa wa kuweza kuongea lugha ya Kiingereza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanafunzi wetu wakimaliza Form six wana option ya kwenda kusoma kwenye vyuo vikubwa kwenye dunia hii. Kama unataka mtoto kwenda kusoma vyuo vikubwa duniani, iwe Harvard, Oxford na vyuo vingine vikubwa kwenye dunia hii, bila ujuzi mzuri wa kuongea, kuandika na kusikia vizuri kugha ya Kiingereza, itakuwa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, ili mtu aweze kufanya biashara za Kimataifa vizuri, lazima awe na uwezo wa kuongea lugha ya Kiingereza. Utakubaliana nami kwamba mikataba mingi ya kibiashara inaandikwa na inakuwa negotiated kwa lugha ya Kiingereza. Ili uwe consultant mzuri kwenye makampuni ya kitaifa na kimataifa, ni lazima uwe na uwezo wa kuongea lugha ya Kiingereza. Pamoja na hayo, hizo ni faida za mtu binafsi lakini nimeamua kufuatilia faida kama Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu kwenye Ilani ya CCM, tunasema tunataka kuleta ajira milioni moja kwenye miaka yetu hii mitano ya uongozi. Lugha ya Kiingereza ni sehemu ya ajira. Watu wetu wakiweza kuongea Kiingereza vizuri, watapata ajira nje ya nchi, kwa hiyo, tutapunguza kugombania ajira za ndani ya nchi. Kama tunataka ajira milioni moja, watu 500,000 wakienda nje ya nchi, 500,000 tutawaajiri ndani ya nchi. Ukiachana na ajira, kuna issue ya remittance kwa diaspora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefuatilia, nika-compare remittance, fedha zinazotumwa na diaspora kutoka nje ya nchi kuja Tanzania, na nika-compare na zinazotoka nje ya nchi kwenda Kenya. Mtashangaa, kwenye nchi ya Tanzania kwa mwaka tunapokea dola milioni 500 kulinganisha na Dola bilioni nne kwenye nchi ya Kenya. Nikafuatilia sababu, nikaambiwa wananchi wa Kenya wana uwezo mzuri wa kujua Kiingereza, hivyo wanaajiriwa kwenye nchi mbalimbalia hasa Ulaya na Marekani. Hatutakiwi kupuuzia suala la uwezo wa Kiingereza kwenye Taifa hili. Kwenye nchi ya Kenya remittance kutoka kwa diaspora ndiyo inaongoza kwenye foreign currency kwenye nchi yao. Kama Tanzania, hatupaswi kupuuza hata kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnafahamu wote, nchi ya Kenya inavyotukimbiza na utalii. Watalii muda mwingine wanapenda kutembelea nchi ambayo hawatasumbuka kuongea lugha ya Kiingereza, ndiyo maana Kenya siku zote inatupiga gap. Tafiti zinasema, nchi ya India sasa hivi inaongoza kwa foreign direct investment kuajiri Wahindi wengi, kwani sasa hivi wana uwezo wa kuongea Kiingereza. Ukiacha India, nenda Kenya, nenda Ghana, nenda South Africa, huwezi kulinganisha na Tanzania. Wawekezaji wengi wanaenda nchi hizo kwa ajili ya uwezo wa kuongea Kiingereza na wananchi wao wanapata faida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuona faida hizo; moja, kwa mtu binafsi; na pili, kwa Taifa, nikaamua sasa kuchimba zaidi, ni wakati gani mtoto wa kitanzania, kwenye umri gani sahihi aweze kujifunza na kuweza kuelewa na kui- master lugha ya Kiingereza? Stadi zinatofautiana, lakini asilimia kubwa zinasema, mtoto anatakiwa kufundishwa lugha ya kigeni hasa Kiingereza akiwa na umri kuanzia miaka sita mpaka miaka 10. Baada ya hapo kweli tunaweza tukamfundisha, lakini hawezi kuongea vizuri kama native speaker. Hawezi kuongea vizuri kama lugha yake ya kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, mtoto asipofundishwa lugha hii ya kigeni hasa Kiingereza, kwenye miaka sita mpaka 10, baada ya hapo hawezi kuongea vizuri lugha ya Kiingereza na hawezi kupata hizi faida ambazo nimezielezea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kujiridhisha kwa hilo pasipo mashaka kabisa, kwamba huo ndiyo umri sahihi, nikaangalia sasa mfumo wetu wa elimu kwenye nchi yetu ya Tanzania.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa.

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba dakika moja.

MWENYEKITI: Malizia sekunde 30.

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mfumo wetu wa kitanzania ni mfumo wa kibaguzi sana. Watoto wa kitajiri, watoto wa viongozi, watoto wa wafanyabiashara ndio wanapelekwa kwenye zile shule, wanasoma lugha ya Kiingereza tangu Darasa la Kwanza. Watoto wa kimasikini, watoto wa wapiga kura wa nchi hii wanapelekwa kwenye zile shule ya Kiswahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kesho nitasimama na Shilingi ya Mheshimiwa Waziri. Kabla ya kumwachia Shilingi, aniambie watoto wake wako kwenye shule gani? Baada ya hapo tuchague mfumo gani tunataka kwenda nao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na ninaunga mkono hoja. Nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa
Spika,nakushukuru kwa nafasi hii. Pili, nimpongeze Waziri, Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara hii ya Maji, kwa namna wanavyopambana kuona namna gani wanatatua changamoto ya maji kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu umuhimu wa maji kwenye jamii zetu. Tunafahamu kwamba kama tunataka jamii au nchi yenye watu wenye afya nzuri tunahitaji maji safi. Kama tunahitaji kuinua kiwango cha elimu wanafunzi wote wa kike na wakiume waweze kwenda kuhudhuria masomo vizuri tunahitaji maji.

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa tunahitaji kuinua kiwango cha uchumi wa nchi yetu, kuzuia magonjwa yasiwasumbue watu na tukapoteza fedha nyingi kwenye kutibu magonjwa, tunahitaji maji safi.

Mheshimiwa Spika, nafahamu juhudi kubwa ambazo Serikali inazifanya kutatua changamoto ya maji na zipo takwimu zinazoonyesha kiwango gani cha maji kinapatikana sasa hivi, lakini kwa uhalisia zaidi ya asilimia 50 bado watu hawana access ya maji safi na salama. Ushauri wangu ni nini? Serikali inabidi sasa itoe kipaumbele kikubwa kwenye Sekta ya Maji.

Mheshimiwa Spika, research zinaonyesha kwamba kutatua changamoto ya maji, kuleta maji safi na salama si kwamba tu muhimu kwa afya, lakini pia tunaona zitanyanyua kiwango cha uchumi kama nilivyosema hapo mwanzo. Pia itasabisha kuwe na Taifa la watu wenye furaha kwa ajili tunapata maji safi, watu wanaoga vizuri kabla ya kwenda kazini asubuhi, kwa hiyo maji ni muhimu sana.


Mheshimiwa Spika, statistics zinasema tuki-invest shilingi moja kwenye Sekta ya Maji pamoja na Usafi wa Mazingira inaweza kuiletea ongezeko la uchumi kwa shilingi 12. Investment ya shilingi moja inaweza kuletea pato la Taifa ongezeko la shilingi 12. Kwa hiyo naomba tujitajidi kuongeza investment kwenye sekta ya maji.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni huu; kama tulivyofanya investment kubwa kwenye standard gauge, tulivyofanya investment kubwa kwenye umeme, tunaona tunajenga bwawa la umeme, kwa nini sasa tusiwe na mradi mkubwa wa kimkakati nchi hii ili kutatua tatizo la Maji Tanzania nzima.

Mheshimiwa Spika, tunaweza tusiwe na fedha za kufanya hivyo, lakini tunaweza tukakopa fedha nje ya nchi au ndani ya nchi kwenye vyanzo mbalimbali kama vile Government Bond tuka-invest kwenye changamoto ya maji ili tuweze kutatua tatizo la maji kwa sasa hivi na hata miaka hamsini ijayo. Halafu tutaendelea kulipa deni hilo pole pole lakini tukiwa na uhakika kwamba changamoto ya maji imekwisha kabisa kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Spika, mradi mkubwa ambao uta- identify tatizo la maji lipo kiasi gani nchi nzima. Mradi mkubwa ambao uta-identify vyanzo vya maji, tumetajiwa Ziwa Victoria, Tanganyika na Maziwa mengine, Mito na kila mahali. Mradi ambao utasambaza maji nchi nzima, tuji-commit sehemu hii tutaendelea kulipa deni lakini tukiwa tunajua kabisa changamoto ya maji imeisha kwenye nchi hii.

Mheshimiwa Spika, naomba nirudi Jimboni kwangu Korogwe. Nashukuru Mheshimiwa Waziri kaka yangu Aweso kwa commitment yake kubwa kuhakikisha anatusaidia kutatua changamoto ya maji pale Korogwe. Korogwe ina changamoto moja, changamoto iliyokuwepo Korogwe kwanza kuna mradi unaoitwa HTM, huu ni mradi wa miaka mingi, mradi huu unasabisha wakati wowote tunapoomba fedha kwa ajili ya maendeleo ya maji, kutatua changamoto ya maji, tunaambiwa mna Mradi wa HTM. Kwa hiyo, tunaomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe anatuleta maji kwenye Mji wa Korogwe bila kuangalia hii HTM. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunamshukuru Waziri kwa sababu kwenye bajeti hii angalau tumepewa hela kidogo, lakini tunaona itatatua angalau changamoto ya maji Korogwe. Nilimwomba milioni 700 kwa ajili ya Kata ya Bagamoyo lakini kwa mwanzo ameniletea milioni 200. Naomba Mheshimiwa Waziri aweze kutumalizia hizo milioni zilizobaki ili kuweza kutatua changamoto ya Maji Korogwe. Tuna imani sana na Mheshimiwa Waziri, tunamwamini na tunajua atatatua changamoto ya maji Korogwe na Tanzania nzima. Mungu ambariki sana.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii na naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi hii kabla sijaongea vitu vyangu vya jimboni naona Mheshimiwa Esther mchango wake uliopita amegusia kidogo kitu ambacho nilitaka kushauri Wizara. Waheshimiwa Wabunge wengi wamesisitiza na wakaonesha kama upo uwezekano wa kutoa maji Ziwa Victoria kupeleka Dodoma; kwa ajili gani tusifikirie kuchukuwa maji kwenye vyanzo vyote vikubwa nchi hii tukavisambaza nchi nzima? Kwa ajili gani tuendelee na vyanzo vidogo vidogo ambavyo havina uhakika nilikaa chini nyumbani mwenyewe nikaanza kufirika na kupiga mahesabu? Nikahisi tufanye kitu kimoja.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri naomba hili ulichukuwe Katibu Mkuu wetu yupo aandike hiki kitu ninachotaka kukishauri Serikali Mheshimiwa Waziri naomba uandike kaka yangu tukae chini tutengeneza business proposal kiasi gani kitatu-cost kuchukuwa maji kutoka vyanzo vyote vikubwa nchi hii, kusambaza nchi nzima kiasi gani kitatutosha kutengeneza treatment plant ambazo zitatosha nchi nzima na kiwango gani cha pesa kitaweza kusambaza mabomba nchi nzima kumaliza ili tatizo kwa wakati mmoja (at once)?

Mheshimiwa Spika, nafahamu hatuna fedha hizo, lakini business proposal hiyo i-identify source of fund, twende tukakope. Nina imani kabisa tukikopa fedha hizo namba moja tutaweza ku-repay ule mkopo kwa kuwa watu watakuwa nchi nzima wanalipa bili za maji na revenue kutoka kwenye maji zitaongezeka, nimepiga mahesabu zitaongezeka mara tano.

Mheshimiwa Spika, tumeambiwa hapa kuna upotevu wa maji asilimia 30 mpaka 45. Kwenye huo mfumo mpya ninaamini kabisa tutakuwa na upotevu wa maji chini ya asilimia 10, kana kwamba tutaweza kuokoa revenue tutaweza kulipa mkopo huo.

Mheshimiwa Spika, nimepiga mahesabu, kwa mfano mwaka huu tumetenga milioni 700. Nina imini bajeti ya Wizara ya Maji kuanzia kipindi hicho ambacho kila Mtanzania atakuwa na maji tutatumia sasa hiyo bajeti ya maji kulipa mkopo na tutakuwa tumeondoa tatizo la maji kabisa nchi hii, na inawezekana Mheshimiwa Waziri. Mimi niko tayari kama utanihitaji. Unafahamu mimi ni mtalaam wa masuala ya fedha, nitashirikiana na wewe au wataalam wengine wa Wizara yako tuweze kutengeneza hiyo business proposal, tuiuze ili tutatue tatizo la maji nchi nzima kwa wakati mmoja. Nakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, naomba nirudi jimboni kwangu. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa miradi mikubwa ambayo ameileta jimboni kwangu. nimshukuru Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kipindi kifupi ambacho ni Mbunge umenipatia milioni 700 kwa ajili ya ujenzi wa maji kwenye Kata ya Bagamoyo, umenipatia fedha kwa ajili ya kumalizia ule mradi ambao unaitwa chechefu wa Longela Relini na Darajani na mwezi huu maji yatatoka. Pia mradi ambao una thamani wa 1.6 bilion uko kwenye hatua za manunuzi tunakushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo bado zipo changamoto chache kwenye Kata ya Kwamsisi, maji yapo lakini ya chumvi Kata ya Manundu Majengo mabomba ni chakavu sana ni yale mabomba ya chuma ambayo yametengezwa tangu mwaka 70; ni chakavu yanavujisha maji sana mjini watu wanakosa maji. Kwenye Kata za Masuguru, Magunga, Mtonga Road Korogwe Mgombezi na kwa Mndolwa wanapata maji kwa shida sana.

Mheshimiwa Spika, lakini ninafahamu, ni imani yangu, na ni imani ya watu wote wa Korogwe kwamba huu Mradi wa Miji 28 ambao ulioasisiwa miaka nane iliyopita nakumbuka kwenye jimbo langu Mbunge alikuwa kaka yangu Nasri; lakini leo baada ya miaka nane tunaenda kuufanyia kazi mradi huo. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri, pia nimshukuru Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kutuhakikisha mradi huo unafanyika.

Mheshimiwa Spika, imani yetu, imani ya watu wa Korogwe, tunaamini mradi huo utaleta maji Korogwe, utaenda kutengeneza matenki sehemu zote zinazohitajika kupelekwa maji, utasambaza mabomba kwenye kata zote na vitongozji vyote na mitaa ya mji wetu. Ninaamini pia mradi huu utatengeneza vizimba vya kuchotea maji kwa wale wananchi wetu ambao hawana uwezo wa kuvuta maji nyumbani mwao.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa tumeambiwa mradi huu utatuletea tu maji kusambaza tutajua wenyewe lakini ndugu yangu juzi umenihakikishia, kwamba mdogo wangu si kweli mradi utaleta maji Korogwe na utasambaza na kihistoria ya changamoto ya maji Korogwe itakuwa imeishia hapo. Mheshimiwa Waziri nakushukuru sana, nilikuwa na hayo mawili machache nataka kuunga mkono hoja, Mungu akubariki sana endelea kuchapa kazi na kupambana sisi ndugu zako tuko nyuma yako. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii, lakini kabla nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa uhai na nguvu. Pia niungane na wenzangu kumshukuru Rais wetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuleta maendeleo nchini kwetu. Kwa kipekee pia niwashukuru Mawaziri wetu, ndugu yangu Bashe pamoja na kaka Anthony kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya kuendeleza Sekta hii ya Kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na muda nina mambo mawili tu ambayo nataka kuchangia leo. La kwanza, ni skimu za umwagiliaji; kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini nina skimu tatu za umwagiliaji. Skimu hizo ni Mahenge, Gou pamoja na Kwamgumi. Kimsingi Jimbo langu ni kati ya majimbo ya mjini wengi tunajishughulisha na biashara, kilimo siyo sana kwa hiyo skimu hizi ni skimu ambazo tunazitegemea kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, skimu hizi zimekuwa na matatizo kwa muda mrefu, watu hasa wa Mahenge na Goho ambao wapo kwenye Kata ya Kwamndolo wamekuwa wakilima mara nyingi mpunga lakini wanapata mafuriko, kwenye miaka mitano tumepata mafuriko zaidi ya mara tatu, nguvu zote walizozitumia kuandaa mashamba hadi wanakaribia kuvuna mafuriko yanakuja mpunga ule unakwenda na maji wote, kwa hiyo ni hasara kubwa wanaipata, kwa juhudi kubwa ambazo wanaziweka kuleta chakula ambacho kinalisha Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana niliiomba Wizara hii na ilinikubalia kwamba itaenda kutujengea skimu zetu, wakasema wataanza na skimu ya Mahenge. Tarehe 5 Julai, 2021 ilitoka list ya skimu ambazo zitaenda kufanyiwa kazi mwaka huu tulionao wa fedha na Mahenge ikiwa skimu Namba Nne kwenye hiyo list, lakini jambo la kushangaza juzi wametoa list ya skimu ambazo zinaenda kufanyiwa kazi na skimu yangu ya Mahenge haipo. Hili jambo limesikitisha sana wananchi wangu pia limenisikitisha mimi sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu gani kimetokea tuliambiwa tunaenda kujengewa skimu ile, nilienda nyumbani Jimboni kwangu nikawatangazia wananchi kwamba hasara sasa ni basi, Serikali imepanga kujenga skimu hizo na tunasubiri fedha kwa mshangao mkubwa list inatoka ya skimu za…

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Timotheo Mnzava.

T A A R I F A

MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba nimpe mzungumzaji taarifa kwamba siyo skimu ya Mahenge tu hata skimu ya Kwamkumbo na ipo barua ya commitment ya Wizara na Tume ya Umwagiliaji kuwa skimu za Mahenge na Kwamkumbo lakini kwenye tangazo la zabuni hazipo, naomba nimpe taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Kimea unaipokea taarifa.

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mikono yangu yote miwili napokea taarifa ya Mheshimiwa Timotheo Mnzava, Mbunge jirani wa Korogwe vijijini. Kimsingi ninajua jitihada kubwa za Kaka yangu Mheshimiwa Bashe, nafamu ni rafiki yangu sana na yeye anafahamu lakini najua jitihada za Ndugu yangu Mheshimiwa Antony najua wanafanya kazi kubwa, lakini kwa hili kesho ninatarajia kushika SShilingi hadi watuhakikishie na watupe majibu kamili kitu gani kinaenda kufanyika. Maana siwezi tena kwenda kurudi Jimboni kwangu mwaka jana niliwaambia inatekelezwa sasa ninawaambia nini, kwamba Serikali haina fedha wakati mwaka jana kulikuwa na list ya skimu 10, mwaka huu zimeletwa list ya skimu 13 za kutengenezwa ya kwangu haipo narudi nawaambia kitu gani wananchi wa Korogwe? Kwa hiyo ninatoa taarifa kwamba kesho nitashika Shilingi mpaka nitakapohakikishiwa siyo ahadi kuhakikishiwa kwamba skimu ya Mahenge itawekwa kwenye list na wananchi wangu wa Mahenge wataenda kujengewa skimu mwaka huu, ninashukuru kwa hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili na la mwisho ambayo ninapenda kuchangia, kilimo kwenye nchi hii, vijana wanatakiwa kuji-engage sana kwenye kilimo lakini changamoto kubwa inayowakumba vijana pia wananchi wetu wa vijijini ni ukosefu wa fedha mitaji, benki zetu zimekuwa haziwezi kukopesha vijana kwa ajili ya kutokuwa na vigezo hasa dhamana. Ninashauri Wizara yetu ianzishe mfuko ambao utakuwa na kazi kubwa mbili. Kazi ya kwanza kusimama kama dhamana hasa kwa vijana wetu wanaomaliza shule, wanaotaka kujiingiza kwenye kilimo hawawezi

kukopesheka kwa hiyo mfuko huo usimame kama dhamana ili waweze kukopeshwa. Pia Wizara imefanya kazi Serikali imefanya kazi kuomba benki nyingi kupunguza riba lakini baadhi ya Benki bado riba ipo juu, kwa hiyo huu mfuko pia utumike kama sehemu ya kupunguza riba, kama benki inakopesha asilimia 10 tunataka vijana wetu wakopeshwe kwa asilimia saba ili asilimia mbili mfuko huu ufanye kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona nchi nyingi zimefanya hivyo nikikutolea mfano nchi ya Ghana ina mfuko huo ambao moja unasimama kama dhamana kwa ajili ya wakopeshwaji lakini namba mbili ku-reduce interest rate endapo benki itakuwa willing kukopesha wakulima lakini interest rate zipo juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu ni hayo mawili, lakini kikubwa sana ni skimu yangu ya Mahenge, kesho nitashika Shilingi endapo hili halitajibiwa, siyo kujibiwa tu Waziri aje na commitment kwamba skimu ya Mahenge itaenda kufanyiwa kazi mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na Mungu awabariki, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia kwenye Wizara hii ya Afya. Awali ya yote, nitumie fursa hii kuushukuru uongozi wa Wizara; moja, dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu, na kaka yetu Mheshimiwa Dkt. Godwin Mollel. Pia nawapongeza Dkt. Self Shekalaghe pamoja na dada yetu Grace Maghembe kwa kazi kubwa wanayoifanya kuhakikisha sekta ya afya kwenye nchi hii inapewa kipaumbele.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, naishukuru na kuipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Sita kwa kazi kubwa ambayo imeifanya hasa kwenye sekta ya afya. Wote tunashuhudia kazi kubwa Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameifanya kwenye sekta hii ya afya. Wote tunashuhudia ujenzi wa hospitali za kikanda, hospitali za rufaa za mikoa, hospitali za wilaya na vituo vya afya na zahanati. Kimsingi, Serikali yetu imefanya kazi kubwa sana, hivyo hatuna budi kuipongeza.

Mheshimiwa Spika, hususan kwenye Jimbo langu la Korogwe mjini, kazi kubwa kwenye sekta ya afya imefanyika, hivyo sina budi kuipongeza Serikali yetu. Mfano, kwenye jimbo langu la Korogwe Mjini kwa kipindi hiki, Mheshimiwa Dkt. Samia akiwa Rais, ameshatujengea vituo vya afya viwili. Moja, kwenye Kata inaitwa Mgombezi na kingine kwenye Kata ya Kwamsisi. Pamoja na hilo, tumejengewa EMD kwenye hospitali yetu ya Wilaya na zahanati karibu kwenye kila Kijiji. Kwa hiyo, hiyo ni kazi kubwa ambayo Serikali yetu imeifanya kwenye sekta ya afya na hatuna budi ya kuipongeza sisi kama wawakilishi wa wananchi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada kubwa ambazo Serikali imefanya, bado ziko changamoto chache ambapo leo napenda kuzieleza ili Wizara yetu hii ya Afya ikapate kuzichukua na kuzifanyia kazi, hasa nitajikita moja kwa moja kwenye Jimbo langu la Korogwe Mjini.

Mheshimiwa Spika, ni kweli tumejengewa vituo vya afya kama nilivyoeleza hapo mwanzo, lakini hadi sasa hivi bado hatujaletewa vifaa tiba. Hivyo naomba Wizara, Mheshimiwa Waziri, basi tupatiwe vifaa tiba ili vituo vile vya afya vizuri kabisa ambavyo Serikali imejenga viende kufanya kazi na wananchi wa Korogwe waweze kunufaika na matunda ya Serikli yao ya Awamu ya Sita.

Mheshimiwa Spika, ukiacha vifaa tiba, changamoto nyingine inayotukumba kwenye Halmashauri yetu kwenye sekta ya afya ni upungufu mkubwa wa watumishi kwenye sekta hiyo. Kwenye Halmashauri yetu ya Korogwe Mjini, ili kukidhi mahitaji ya sekta ya afya tunatakiwa kuwa na wafanyakazi zaidi ya 700, lakini hadi sasa tuna wafanyakazi chini ya 300, hivyo tuna upungufu wa wafanyakazi 400.

Mheshimiwa Spika, upungufu huo hasa kwa wataalam wa maabara, wauguzi pamoja na wafamasia. Hivyo, tunaishauri na tunaiomba Serikali yetu ikapate kuendelea kuajilri watumishi wa afya kama ilivyofanya hapo awali ili wakapate kuweza kuongezeka na vituo vile ambavyo tumejenga vikapate wataalamu ili wananchi wetu waweze kuhudumiwa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo napenda kuizungumzia leo, ni changamoto ya usafiri. Kwenye Halmashauri yetu ya Korogwe, kwenye jimbo langu, kwenye hospitali zetu tuna uhaba mkubwa sana wa usafiri hasa ambulance lakini pamoja na magari mengine ya administrative supervision na kazi nyingine. Hivyo, tunaiomba Serikali ikapate Kwenda kutupatia ambulance kwa ajili ya vituo hivi vya afya lakini pamoja na hospitali yetu ya wilaya.

Mheshimiwa Spika, changamoto nyingine ambayo napenda kuieleza kwenye sekta ya afya kwenye jimbo langu ni uchakavu wa miundombinu. Nilikwisha kueleza hapa Bungeni si mara moja kwamba, Hospitali yetu ya Korogwe, hospitali yetu ya wilaya ni chakavu sana na imechoka ilijengwa tangu mwaka 1952 na haikidhi kabisa matakwa ya kuhudumia watu wetu kwa kipindi hiki. Nimekwisha kuomba mara nyingi lakini nipende kuishukuru Serikali kupitia Wizara ya TAMISEMI, kwenye bajeti hii imetutengea shilingi milioni 900 kwa ajili ya ukarabati wa hospitali ile.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na ushauri kidogo mahali hapa, naomba Waziri wa Afya akae na Waziri wa TAMISEMI, ili wapate kukubaliana jambo hili. Hospitali yetu ya Korogwe ambayo ni chakavu na hospitali nyingine kwenye nchi hii, hospitali zile kongwe na chakavu zimepelekewa fedha kwa ajili ya ukarabati shilingi milioni 900.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu, fedha hizi zisiende kufanya ukarabati hatutaona value for money, fedha hizi ziende kujenga majengo mapya. Safari hii mmetupatia milioni 900 basi tucahgue majengo gani yatajengwa na milioni 900 safari hii na mwakani mtupatie nyingine zikajenge majengo mengine. Mkisema muende kukarabati hela zitisha na hamna kitu kitakacho onekana pale. Hatutapata value for money kwa ajili vijengo ni vidogo designing yake ni ya miaka 60 iliyopita, tunakwenda kukarabati kitu gani?

Mheshimiwa Spika, hivyo ninamuomba Waziri wa Afya akae na akabualiane na Waziri wa TAMISEMI, wakubaliane ili hizi hela zisiende kufanya ukarabati. Watu watakwenda kupiga piga rangi, watabadilisha mabati, tiles kidogo hamna kitu kitakachoonekana baada ya miaka miwili tutakuwa na uhitaji mwingine. Hivyo, fedha hizi ziende kujenga majengo mapya naamini miaka miwili mpaka mitatu tutapata hospitali mpya kabisa ambazo zitakidhi mahitaji ya karne hii, sio kukarabati hozpitali za miaka 50 iliyopita. Huo ndio ulikuwa ushauri wangu.

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Mheshimiwa Waziri, naomba hili ulielewe vizuri dada yangu, najua wewe ni mpambanaji na unaweza. Serikali imefanya pakubwa, imejenga majengo, inaajiri wataalam, vifaa tiba na hadi sasa hivi tuna madawa ya kutosha.

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyokuwa nayo ni malalamiko ya wagojwa juu ya wauguzi na wataalam kwenye hospitali zetu. Kumekuwa na malalamiko mengi kwenye hospitali zetu za halmashauri wagonjwa wanalalamika hawawi–treated vizuri na wauguzi wetu. Hivyo, Mheshimiwa Waziri, ushauri na rai yai yangu kwako, hebu fanya uchunguzi kwenye hospiali za Halmashauri ya Korogwe Mjini lakini na hospitali nyingine kwenye taifa hili uweze kuangalia ni kwa ajili gani wagonjwa wanalalamikia wauguzi.

Mheshimiwa Spika, kama shida ipo, basi mfuatilie mjue ni shida gani inawezekana wauguzi wetu wanakuwa over worked, inawezekana watu ni wachache au hawapati stahili zao vizuri. Basi muende kufuatilia changamoto hizi ili muweze kuzitibu ili waweze kuhudumia wananchi wetu vizuri. Mnafanya kazi kubwa lakini wagonjwa wetu wasipohudumiwa vizuri itakuwa ni kazi bure, hivyo Mheshimiwa Waziri nakuomba.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo ninatamani pia wawe wanapewa elimu ya mara kwa mara ethical education na vitu vingine. Waambiwe ni namna gani wao ni muhimu kwenye afya ya watanzania. Mheshimiwa Waziri, hayo ni machache ya kwangu niliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, nilikuwa na hayo machache kwenye bajeti hii ya Wizara ya Afya. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi kuweze kuchangia kwenye bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote napende kumpongrza Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, ambae ndiye Amiri Jeshi Mkuu na Kiongozi mkubwa wa Majeshi haya yote, niendelee kumpongeza kwa kazi kubwa ambayo anaifanya kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ninatumia fursa hii kumpongeza Kiongozi wa Wizara hii Waziri wetu Mheshimiwa Innocent Bashungwa, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya pia tumpongeze Katibu Mkuu, Ndugu yetu Dkt. Faraji Mnyepe kwa kazi kubwa ambayo anaifanya na kwa ushirikiano wake mkubwa ambao anautoa kwa Kamati na Watanzania kwa ujumla. Niwapongeza pia Majemedari na Makamanda wote ndani ya nchi hii ambao wanafanya kazi kubwa kuhakikisha nchi yetu inaendelea kuwa salama.

Mheshimiwa Spika, nina mambo machache sana ya kuchangia leo, jambo la kwanza, jambo hili limezungumzwa na Wabunge wengi, naomba Waziri wa Fedha apate kutuambie anafanya nini juu ya suala hili la changamoto ya kikodi.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kazi kubwa ambayo Jeshi letu linafanya, tuwasaidie hawa watu waendelee kuifanya kazi yao vizuri kwa kuwapatia msamaha wa kodi asilimia 100. Waziri wa Fedha, akae chini na Wizara hii wapate ku–define vifaa vya kijeshi ni nini? Vifaa vya kijeshi siyo bunduki au risasi peke yake. Kitu chochote kinachoagizwa na Jeshi letu hivyo ni vifaa vya kijeshi. Hivyo, Wabunge tunaomba ndugu zetu hawa wapatiwe msamaha wa asilimia 100. Wabunge wengi wamezungumza sitaki kuongea sana kwenye detail kwa sababu najua Waziri wa Fedha atakuwa amekwishachukua atalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, suala la pili, limeongelewa na ndugu yangu Chumi hapa mwisho. Hawa ndugu zetu ili kuhakikisha vifaa vyao havikai bandarini muda mrefu, wametengeneza bonded warehouse zao lakini TRA bado Inawakatilia kupeleka vifaa vyao kwenye bonded warehouse zao wakiwa wanaendelea na process za clearing.

Mheshimiwa Spika, tunaomba watu wa TRA waweze kutoa go ahead Jeshi letu likapate kutumia bonded warehouse zao kuhifadhi mizigo yao wakiwa wanafanya process za kufanya clearing. Vifaa vyao kukaa kwa muda mrefu pale kwanza ni aibu kwa Taifa letu, kwa watu ambao wanajitoa kwa Taifa hili kuweza kuzuia mizigo yao halafu iko pale bandarini.

Mheshimiwa Spika, mwisho, muda mwingine huwa hatufahamu wanaagiza vitu gani kwa matumizi gani? Siku moja tutakuja kukimbiana pale bandarini inawezekana kuna vitu havistahili kukaa kwa muda mrefu pale kwenye bandari yetu, waruhusuni watu hawa kwa kuwa ni ngumu kuweza kumwelezea kila mtu kitu gani kiko kwenye ma - container yao kwa ajili ya issue za kiusalama, waruhusiwe wawe na bonded warehouse zao vifaa vyao vikija vyote vihifadhiwe huko kama mnataka watu wenu wa TRA wawe huko clearing ifanyike vifaa vyao vikiwa kwenye maghala yao na siyo ndani ya bandari yetu pia itapunguzia mzigo bandari yetu ambayo tunataka iwe ya kisasa na ihudumie mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye suala la kikodi ninaamini kabisa Waziri wa Fedha leo katika kuhitimisha ataliongelea suala hili na atatuhakikishia kwamba moja, kutakuwa na msamaha wa asilimia 100 lakini pili, wataruhusu Jeshi letu liweke vifaa kwenye bonded warehouse zao. Hivyo ni vitu viwili ambavyo nilitaka kuchangia.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho pia limeongelewa na watu wengi ni Shirika la Nyumbu. Naomba niongelee kwa uchache Shirika hili la Nyumbu. Kwanza, napenda kuipongeza Serikali hasa viongozi wetu waasisi wa Taifa hili kwa kuwa na maono haya makubwa ya kuwa na shirika hili. Nahisi watu wengi hawafahamu ndoto za Rais wetu wa Kwanza kuanziasha shirika hili. Alikuwa anatamani siku moja Tanzania iwe inajitosheleza kwenye masuala ya magari, vifaa vya kijeshi, kila kitu kifanyike ndani ya nchi yetu, lakini changamoto ya Serikali yetu baada ya hapo hatukuwa committed kwenye shirika lile. Ninaiomba Serikali iwe Committed ili shirika hili liende mbali zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza viongozi wa Shirika hili. Shirika hili limejiongezea uwezo mkubwa sana, ukifika pale utaona mambo makubwa ambayo yanafanywa kwenye shirika lile. Wanatengeneza magari ya Kijeshi, wanatengeneza magari ya zima moto, wanatengeneza vifaa vya nyumbani, majiko na vitu vingine lakini kikubwa zaidi wanatengeneza hadi vifaa vya kilimo ambapo nchi yetu inatamani kupeleka suala la kilimo mbali zaidi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iwe committed iwapeleke fedha mimi ninaamini kabisa nchi yetu itafika mbali sana tukiamua kuwekeza kwenye shirika hili. (Makofi)

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Nani mtoa taarifa? Mheshimiwa Ali Mohamed.

TAARIFA

MHE. ALI JUMA MOHAMED: Mheshimiwa Spika, napenda nimpe taarifa mchangiaji anaeendelea kwamba licha ya changamoto mbalimbali na mafanikio ambayo yanatokea nchini kutokana na Jeshi letu, lakini Jeshi letu limekuwa likiijengea sifa sana nchi yetu ya Tanzania hasa pale linaposhiriki katika mission mbalimbali za Kimataifa. Hii imepelekea kupata sifa kwenye Jumuiya ya Kimataifa, sasa ikiwa Jumuiya ya Kimataifa inathamini sana Jeshi letu, kwa nini Serikali yetu ishindwe kutoa uwezo wa kifedha kwa ajili ya Jeshi letu? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Kimea, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa kwa mikono yote miwili. Kwa hiyo, ninachotaka kusisitiza hapa Serikali yetu iwe committed kwenye shirika hili ninaamini kabisa tutaenda mbali.

Mheshimiwa Spika, tukiamua kwenye nchi hii kwamba: (i) Magari yote ya zima moto yasiagizwe kutoka nje ya nchi, yatengenezwe kwenye shirika hili. (ii)Magari yote ya kuzolea taka kwenye nchi yetu yaagizwe kutoka kwenye shirika hili. Tukisema ambulance zote zitengenezwe kwenye shirika hili, magari ya Majeshi yetu ya Jeshi la Polisi, Magereza yote yaagizwe toka shirika hili, ninaamini shirika linao uwezo, tumetembelea pale tumeona, tukiamua ku - invest pale ninaamini watatengeneza vitu kwa ajili ya nchi yetu na tutaweza kuuza hata nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, hivyo, ninaiomba Serikali iweze kulipatia fedha shirika hili nina amini kabisa katika uchumi wa nchi yetu kwanza litatengeneza ajira nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa na hayo machache ya kuchangia. Ninapenda kuunga mkono hoja hii na tupo pamoja Wanakamati tutaendelea kushirikiana nao. Ahsante sana kwa kunipa muda huu. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii jioni ya leo ya tarehe 09/11/2023, na mimi kuchangia kwenye Mpango huu wa mwaka 2024/2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijatoa ushauri wangu hasa nimejielekeza kwenye Sekta ya Kilimo. Ninaomba nitumie fursa hii kueleza mambo machache sana ya nyumbani kwetu nikimaanisha kwenye Jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zaidi ya miaka mitatu kama siyo minne tuliahidiwa kujengewa barabara kwa kiwango cha lami, barabara ambayo inaunganisha Majimbo muhimu matatu kwenye Mkoa wa Tanga Jimbo langu la Korogwe Mjini, Jimbo la ndugu yangu Timotheo Mnzava Korogwe Vijijii lakini Kimbo la Kaka yangu Dunstan Kitandula. Barabara hii tumeahidiwa mara nyingi, Serikali ilituahidi kwamba mwaka huu wataenda kumaliza upembuzi yakinifu ili barabara ile iweze kutangazwa. Mwezi wa Sita walituahidi watamaliza mwezi wa Sita umepita hawajamaliza, wakasema mwezi wa Tisa, mwezi wa Tisa umepita haijamalizika baada ya hapo wanatuambia mwezi wa Kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ahadi zimekuwa nyingi tunaomba Serikali itimize ahadi hiyo, upembuzi yakinifu umalizike barabara hiyo itangazwe ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami kama tulivyoahidiwa. Kibaya zaidi Mheshimiwa Rais pamoja na Waziri Mkuu kwa nyakati tofauti walimuahidi Kiongozi wetu mkubwa kabisa wa dini kwenye nchi hii kwamba wataenda kujenga barabara ile, Mufti Mkuu wa Tanzania. Tunaweza tukaacha kutimiza ahadi lakini mpaka kwa Viongozi wetu hawa wakubwa wa dini haileti picha nzuri. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kwenda kufanyia kazi barabara ile haswa kipindi hiki cha mvua imeharibika sana haipitiki kwa hiyo waende kuingalia na waone namna gani wanawasaidia wananchi wa Korogwe Mjini kwenda Magoma, kwenda Mabwepande ambayo inaunganisha Majimbo matatu muhimu na ndugu zangu Mheshimiwa Kitandula na Mheshimiwa Mnzava pamoja na mimi tumekuwa tukiliongelea mara nyingi. Ahsante nimeanza na utangulizi huo.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu mkubwa ni kwenye Sekta ya Kilimo siku ya leo, nimejipanga kuchangia sehemu saba kwenye Sekta ya Kilimo, muda ukinitosha nitachangia zote muda ukiniishia katikati hapo nitakapoishia nitaishia hapohapo, kikubwa ninachotaka kuchangia moja ni Mikopo kwenye sekta ya kilimo, riba ya mikopo ya sekta ya kilimo, pembejeo kwenye sekta ya kilimo, bima ya kilimo, masoko, miundombinu ya umwagiliaji, uongezwaji wa thamani kwenye mazao ya kilimo. Hayo ni mambo saba ambayo nataka kuchangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na jambo la kwanza ambalo ni mikopo kwenye sekta ya kilimo. Kwanza nitumie fursa hii kumshukuru Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan jinsi anavyoendelea kuongeza bajeti kwenye sekta ya kilimo tunaona miundombinu mingi kwenye sekta ya kilimo ikiwemo miundombinu ya umwagiliaji ikijengwa siku hadi siku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ni uwekezaji mkubwa ambao Mama Samia Suluhu Hassan anaifanya kwenye sekta ya kilimo lakini bado tuna changamoto kubwa kwa wakulima wa nchi hii kukosa mitaji ili waweze kujikita kwenye sekta ya kilimo. Tumekuwa tukihubiri sana kwamba Benki zetu za Biashara pamoja na Benki yetu ile ya Kilimo inatoa mikopo kwa wananchi lakini kwenye ground hali haiko hivyo, vijana wetu, wamama na wakulima wadogo imekuwa ni vigumu sana kupata mikopo kwenye taasisi hizi za mikopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali moja kuendelea kuongeza bajeti au fedha kwenye Benki yetu ya Kilimo ili kuhakikisha tunaongeza wigo wa wananchi wa Kitanzania ambao wanapenda kulima wapate mikopo ili waendeleze sekta ya kilimo. Nilikwisha kushauri kwenye Bunge hili kwamba hizi Benki za Kibiashara zinafanya biashara na hazitaki kupata hasara.

Mheshimiwa mwenyekiti, sekta ya kilimo ni kati ya sekta ambazo risk iko kubwa hivyo ili kuongeza appetite ya hizi benki kuweza kukopesha wakulima ni lazima Serikali ije na bajeti na fund kuwepo na mfuko ambao risk ambayo inatokana na kukopesha sekta ya kilimo iwe inakuwa covered na hiyo fund ambayo Serikali imeiweka. Tukifanya hivyo benki zetu za kibiashara zitaongeza mikopo kwa wakulima kwa kuwa wanajua endapo wakulima wata-default mikopo hiyo kuna fund kutoka Serikalini ambayo ita-cover risk hiyo. Nilikwisha kushauri ninaomba ndugu zetu hawa Waziri wa Fedha pamoja na Waziri wa Mipango waone namna Mfuko huo unakuja ili kuongeza mikopo kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namba mbili kama nilivyosema ni riba. Tunashukuru Serikali kupunguza riba kwenye sekta ya kilimo kushuka mpaka single digit asilimia tisa lakini bado tunaweza tukafanya zaidi riba ikapate kupungua benki zetu zinapata faida kubwa, tupunguze riba kwenye sekta ya Kilimo ili tupunguze gharama ya kilimo, hilo ni jambo la pili tuangalie namna tunapunguza riba kwenye sekta ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ambalo nataka kuchangia ni pembejeo kwenye sekta ya kilimo hasa pembejeo muhimu kama mbegu pamoja na mbolea. Watanzania wengi, wakulima wengi wa nchi wanashindwa kuingia kwenye kilimo kwa ajili ya kukosa Pembejeo muhimu haswa Mbegu. Mheshimiwa Bashe atakuwa shahidi mwaka jana msimu uliopita nilikuwa nikimsumbua sana wananchi wangu wa Korogwe Mjini ambao walikuwa wanatafuta mbegu bora za mahindi kwa ajili ya kupanda hawakupata mbegu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba Serikali ije na mkakati ili pembejeo hizi muhimu mbolea na mbegu ziwe za kutosha nchi hii na gharama ipate kupungua lakini ushauri wangu angalau najua watu wengi wanaweza kupinga kusema gharama ni kubwa lakini nchi hii ina uwezo wa kufanya mbegu kuwa bure kwenye nchi hii, mtu yeyote ambaye anataka kulima akapate kupata mbegu bure. Kama haiwezekani basi wakati wa kilimo wananchi wakopeshwe mbegu wakati wa mavuno wapate kurudisha fedha hizo walizokopeshwa kwa ajili ya kupata mbegu. Kama hilo haliwezekani basi ruzuku kwenye mbegu na mbolea ipate kuongezeka ili gharama ya pembejeo hizi muhimu kwenye nchi hii zikapate kushuka ili gharama ya kilimo ikapate kupungua, hilo ni jambo langu la tatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la nne la muhimu ni bima kwenye sekta ya kilimo. Watanzania wakulima ambao wamekuwa wakilisha Taifa hili kwa muda mrefu, wamekuwa wakilima bila uhakika, wanalima kwa kubahatisha, hawajui watavuna au hawatavuna. Wakulima wamekuwa wakiingiza fedha nyingi wamekuwa wanaingiza nguvu nyingi kwenye kilimo..

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa

MWENYEKITI: Taarifa

TAARIFA

MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi nimpe taarifa. Kwa bahati mbaya wakulima hata watakapovuna hayo mazao ambayo wamelima kwa shida, Serikali ikinunua haiwalipi fedha kwa wakati.

MWENYEKITI: Hiyo ni taarifa kweli? Endelea na mchango. (Kicheko)

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru. Kwa hiyo nilichokuwa nataka kuongelea hapa wakulima wamekuwa wakiingiza nguvu, wakiingiza fedha kwenye kilimo lakini kukija na majanga kama wadudu, majanga kama ukame na vitu vingine wanakuwa wanapoteza kila kitu kwa kuwa hatuna bima ya kilimo kwenye nchi hii, tuna makampuni machache sana yanayotoa bima na hawa wanatoa bima ni aghari sana wananchi hawawezi ku-afford lakini watanzania wengi hawana uelewa wa jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoshauri moja ni kwamba, tuje na mikakati ambayo itasaidia kuwa na taasisi nyingi zinazotoa bima lakini bima hizo zikapate kutolewa kwa bei rahisi ili wakulima wengi wakapate ku-cover risk ambazo zinatokana na kilimo. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante kengele ya pili.

MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja. (Makofi)