Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Saashisha Elinikyo Mafuwe (19 total)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Mashamba yaliyochukuliwa na Vyama vya Ushirika Wilaya ya Hai yameshindwa kuendelezwa huku Wananchi hawana mashamba ya kulima:-

Je, kwa nini Serikali isiyarudishe mashamba hayo kwa Wananchi?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Kilimo, naomba kumjibu Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Hai ina jumla ya mashamba 17 yanayomilikiwa kihalali na Vyama vya Ushirika. Mashamba hayo yana jumla ya ekari 10,139.5 kati ya hizo ekari 7,769 zimekodishwa kwa wawekezaji na ekari 580 zimepewa taasisi mbalimbali ili kuweza kuongeza mapato katika Vyama vya Ushirika husika na jumla ya ekari 1,789 zinatumika na wanachama wa Vyama vya Ushirika kwa shughuli za kilimo.

Mheshimiwa Spika, kama kunatokea kusuasua kwa matumizi ya mali za Vyama vya Ushirika ikiwemo mashamba, ni jukumu la Serikali kusaidia Vyama hivyo kuendeleza mali hizo. Mathalani, Aprili, 2020, Tume ya Maendeleo ya Ushirika ilituma Timu ya Wataalam Wilayani Hai kufanya tathmini ya mashamba yote yanayomilikiwa na Vyama vya Ushirika ikiwa ni pamoja na uwekezaji unaofanyika na kutoa ushauri kwa vyama hivyo kuhusu uwekezaji husika.

Mheshimiwa Spika, baada ya tathmini iliyofanyika, mwezi Julai 2020, Serikali kupitia Tume ya Maendeleo ya Ushirika ilitoa Mwongozo kwa Vyama vya Ushirika vinavyomiliki mashamba kuyaendeleza na kufanya uwekezaji kwenye sekta ya kilimo ili kuwanufaisha wanachama na kwa sasa mashamba yote yanatumika.

Mheshimiwa Spika, aidha, Tume ya Maendeleo ya Ushirika inaendelea kufanya urasimishaji wa mali zote ikiwa ni pamoja na mashamba yanayomilikiwa na Vyama vya Ushirika na kuweka mikakati endelevu ili mali hizo ziweze kutumika kwa manufaa ya wanachama wa ushirika na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Serikali haina mpango wa kuchukua mashamba yanayomilikiwa na Vyama vya Ushirika, bali itaendelea kusimamia na kushauri vyama kuendeleza mashamba hayo kwa kutekeleza mipango ya uwekezaji itakayonufaisha Wanachama wa Vyama vya Ushirika. Aidha, hatua za kisheria zitachukuliwa dhidi ya wanachama au viongozi wa Vyama vya Ushirika watakaobainika kutumia mashamba hayo kwa maslahi binafsi.
MHE. SAASISHA E. MAFUWE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi aliyotoa Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni ya kuongeza watumishi 403 wa afya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba sasa kujibu swali la Mheshimiwa Saasisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka ya 2015 hadi 2020, Serikali imeajiri jumla ya watumishi 14,479 wa kada mbalimbali za afya. Katika Mwaka wa Fedha 2020/ 2021 Serikali inatarajia kuanza kuajiri watumishi 75 wa kada mbalimbali za afya kwenye Wilaya ya Hai kwa ajili ya hospitali ya wilaya moja, vituo vya afya sita na zahanati 28 ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa ahadi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, lini ni Serikali itatekeleza ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais wakati wa Kampeni ya kumaliza mgogoro wa ardhi uliopo kati ya wananchi na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege KIA?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa mbele baada ya kupewa kura za kutosha na wananchi wa Tarime Vijijini, naomba niwashukuru sana kwa ushirikiano. Pia, namshukuru Mungu kwa yote yaliyotokea na namshukuru sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kuniamini na kunipa nafasi ya kuwa Naibu Waziri, Ofisi ya Ujenzi na Uchukuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: - (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka 1969 Serikali ilitenga eneo lenye ukubwa wa ekari 11,085 kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanja cha Ndege cha Kimataifa cha Kilimanjaro (KIA). Eneo hilo lilipimwa mwaka 1989 kwa ramani ya upimaji Na. E255/18 iliyosajiliwa na namba 231264 inayofahamika kama FARM No.1 lenye Hati namba. 22270 iliyotolewa 20 Machi, 2005.

Mheshimiwa Spika, mnamo mwaka 2001 Serikali ilibaini kuwepo kwa baadhi ya wananchi kutoka vijiji vinavyopakana na KIA vya Sanya Station, Chemka, Tindigani na Mtakuja vilivyopo Wilaya ya Hai na Vijiji vya Majengo, Samaria na Malula vilivyopo Wilaya ya Arumeru kuingia kwenye eneo la KIA na kuweka makazi ya kudumu.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilichukua hatua za kufanya tathmini shirikishi wa mali za wananchi ili kuwaondoa kwa lengo la kutimiza azma ya Serikali kuendeleza KIA na pia kulinda usalama wa Kiwanja. Katika utathmini huo, ilibainika kwamba ndani ya eneo hilo kuna kaya 289 zenye thamani ya fidia iliyotakiwa shilingi 426,020,500/=. Fedha za kulipa fidia hizo hazikuwepo wakati huo, kwa hiyo, fidia haikulipwa.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2013, 2018 na 2019 kwa nyakati tofauti, Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa kushirikisha TAMISEMI, Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Fedha na Mipango, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro na Arusha, Ofisi ya Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wa Wilaya za Hai na Arumeru imekuwa ikishughulikia suala hili kwa kushirikiana na uongozi wa vijiji husika ili kupata suluhu kwa kubaini idadi ya kaya zenye makazi ya kudumu katika eneo la KIA na kufanya tathmini upya.

Mheshimiwa Spika, mwezi Juni, 2018 zoezi la uwekaji wa alama lilianza ambapo Vijiji vya Majengo na sehemu ya Kijiji cha Mtakuja viliwekwa alama za kudumu. Vijiji vya Samaria na Malula vilivyopo Wilaya ya Arumeru, Vijiji vya Tindigani na Sanya Station katika Wilaya ya Hai vilikataa kutoa ushirikiano kwa Timu ya Wataalam kwa kukataza wataalam katakata kuingia katika eneo hili.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali imejipanga kukamilisha zoezi hili kwa kurudishia mipaka ya kudumu ya KIA na kubaini idadi ya kaya zilizopo ndani na kufanya tathmini upya na kupata kiasi ambacho kinatakiwa kulipwa ili zoezi hili liweze kumalizika. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, zao la Kahawa limekuwa likilimwa kwa wingi katika Jimbo la Hai lakini zao hili kwa sasa limekosa tija.

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati sahihi wa kufufua zao hilo katika Jimbo la Hai?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri wa Kilimo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshaanza kuchukua hatua za kufufua zao la Kahawa katika mkoa wa Kilimanjaro likiwemo Jimbo la Hai. Hatua hizo zinatokana na kushuka kwa uzalishaji kutoka tani 3,486 mwaka 2014/2015 hadi kufikia tani 1,428 mwaka 2020/2021 sawa na asilimia 59. Kushuka huko kumechangiwa na baadhi ya wakulima kuacha kuyahudumia mashamba kulikosababishwa na kuzorota uliokuwa muhimili wa uzalishaji wa kahawa Mkoani Kilimanjaro. Sababu nyingine iliyochangia ni mabadiliko ya tabia nchi yaliyopelekea ukame na kukosekana kwa maji ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kufufua zao la kahawa Mkoani Kilimanjaro likiwemo Jimbo la Hai kwa kufanya mambo yafuatayo:-

(i) Kukifufua na kukijenga upya Chama Kikuu cha Ushirika wa Kahawa Mkoa wa Kilimanjaro KNCU kwa kurejesha mali zilizouzwa kiholela na kuwachukulia hatua za kisheria waliosababisha ubadhilifu wa mali za Ushirika;

(ii) Kuimarisha Taasisi ya Utafiti wa kahawa Tanzania (TaCRI) kwa kuipa rasilimali ili itekeleze majukumu yake kikamilifu ya utafiti wa zao la kahawa na uzalishaji wa miche bora ya Kahawa;

(iii) Kuhamasisha upandaji wa miche bora ya kahawa kwa kuwauzia wakulima kwa bei ndogo ya shilingi 100 ambapo jumla ya miche 1,203,300 imesambazwa kwa wakulima 3,270 na miche 810,000 imesambazwa katika Wilaya ya Hai;

(iv) Kumaliza migogoro ya kimkataba iliyopo kati ya Vyama vya Ushirika na Wawekezaji katika mashamba 17 ya kahawa; na

(v) Kufufua na kuimarisha viwanda 12 vya kati vya kuchakata kahawa CPU vinavyomilikiwa na wakulima wadogo, Viwanda vyote hivyo vipo katika Wilayani Hai.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua hizi zinazochukuliwa na Serikali zitachochea ufufuaji wa zao la kahawa Mkoani Kilimanjaro ikiwemo Wilaya ya Hai na maeneo mengine nchini.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI K.n.y. MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza kutekeleza ahadi iliyotolewa na Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa Barabara ya Bomang’ombe – Rudugai – Chekimaji – Kikafu chini – Kawaya – Mijengweni – Shing’oro Mferejini hadi Makoa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Bomang’ombe – Rudugai – Chekimaji – Kikafu Chini – Kawaya – Mijengweni hadi Shing’oro Mferejini hadi Makao zimesajiliwa kwa majina ya Bomang’ombe – Kikafu Chini na ina urefu wa kilomita 26.53.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara ya Shing’oro – Mijengweni hadi Makoa yenye urefu wa kilomita 12.7 na Barabara ya Mferejini – Makoa yenye urefu wa kilomita 21 ni barabara muhimu katika Halmashauri ya Hai na zinahudumiwa na Wakala wa Barabara Vijijini wa Wilaya ya Hai. Serikali inatambua kuwa barabara hizi ni miongoni mwa barabara zilizoahidiwa kujengwa kwa kiwango cha lami katika ahadi za Rais na Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kutekeleza ahadi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuzifanyia matengenezo barabara hizo ili kuhakikisha zinapitika katika majira yote ya mwaka. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, TARURA Halmashauri ya Hai iliidhinishiwa shilingi milioni 72 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Bomang’ombe – Kikafu Chini kipande chenye urefu wa kilomita 14 kwa shilingi milioni 35 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Shing’oro – Mijengweni kipande chenye urefu wa kilomita 4 na sShilingi milioni 67.5 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Mferejini – Makoa kipande chenye urefu wa kilomita 6.4 ambapo matengenezo ya barabara hizo yanaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022, TARURA Halmashauri ya Hai imetengewa jumla ya shilingi milioni 628.2 kwa ajili ya matengenezo ya Barabara ya Bomang’ombe – Kikafu Chini kipande chenye urefu wa kilomita 10 na boksi kalvati moja la Shing’oro – Mijengweni kipande chenye urefu wa kilomita 8 na ujenzi wa barabara ya Mferejini – Makoa kwa kiwango cha changarawe kwa kilomita 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi na kutekeleza ahadi za Rais za ujenzi wa barabara za lami katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo Halmashauri ya Hai.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Ujenzi wa Barabara za Kwasadala – Jiweni, Mashua - Shirinjoro –Mijongweni, Kalali – Nronga, Arusha Road – Mlimashabaha –Sanya Stastesheni pamoja na Kwasadala – Uswaa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara za Kwasadala –Jiweni – Mshua, barabara ya Shirinjoro – Mijengweni, barabara ya Kalali – Nronga, Arusha Road - Mlima Shabaha – Sanya Stastesheni pamoja na Kwasadala – Uswa zimesajiliwa kwa majina ya Kwasadala - Mshua yenye urefu wa kilomita 35.06, barabara ya Shirinjoro - Mijongweni yenye urefu wa kilomita 12.71, barabara ya Kalali - Nronga yenye urefu wa kilomita 6.04, barabara ya Somali - Tindigani yenye urefu wa kilomita 12.00 na Barabara ya Kwasadala - Uswaa yenye urefu wa kilomita 9.87.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali kupitia TARURA, Halmashauri ya Wilaya ya Hai imezifanyia matengenezo barabara za Kwasadala - Mashua kilomita 14, Shirinjoro - Mijongweni kilomita 5, Kalali -Nronga kilomita 5 na barabara ya Kwasadala - Uswaa kilomita 5 kwa gharama ya shilingi milioni 157.5. Katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetenga shilingi milioni 189.35 kwa ajili ya matengenezo ya barabara za Kwasadala - Mshua kilomita 17, Shirinjoro - Mijongweni kilomita 4, Kalali-Nronga kilomita 5 na barabara ya Kwasadala - Uswaa kilomita 9. Matengenezo ya barabara hizo yanaendelea na yanatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 barabara hizo zimetengewa shilingi milioni 123 kwa ajili ya matengenezo ya vipande vyenye jumla ya urefu wa kilomita 30.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itabadilisha Muundo wa Utumishi wa Maafisa Utumishi/Utawala na Walimu ili waweze kuanza na Daraja E kama ilivyo Kada ya Sheria na nyinginezo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinkyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Miundo ya Maendeleo ya Utumishi ya Kada mbalimbali inayotumika sasa katika Utumishi wa Umma iliandaliwa kwa kuzingatia matokeo ya zoezi la Tathmini ya Kazi iliyofanyika kuanzia mwaka 1998 hadi 2000. Aidha, Miundo husika ilianza kutekelezwa mwezi Julai, 2003.

Mheshimiwa Spika, matokeo ya zoezi la tathmini ya kazi iliyoainisha uzito wa majukumu ya kada mbalimbali katika utumishi wa umma na yaliyotumika kama msingi wa kupanga vianza mshahara kwa watumishi wa umma wa kada mbalimbali wakiwemo Maafisa Utumishi na Utawala ambao wanaanza na ngazi ya mishahara ya TGS D, walimu Daraja C yaani walimu wenye shahada ambao wanaanza na ngazi ya mshahara TGTS D na Maafisa Sheria ambao wanaanza na ngazi ya mshahara ya TGS E.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2015 hadi 2017 Serikali iliendesha zoezi lingine la tathmini ya Kazi katika Utumishi wa Umma ambalo lililenga kubaini uzito wa majukumu kwa kada mbalimbali. Katika kuoanisha na kuwianisha viwango vya mishahara vya watumishi katika Utumishi wa Umma, Serikali itatumia matokeo ya mapendekezo ya zoezi hilo kupanga vianzia mshahara vya kada mbalimbali ikiwa ni pamoja na Maafisa Utumishi na Utawala na Walimu kwa kuzingatia uwezo wa kibajeti. Naomba kuwasilisha.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kiwanja cha Michezo katika Wilaya ya Hai?
NAIBU WAZIRI WA UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saasisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sera ya Maendeleo ya Michezo ya mwaka 1995, Ibara ya 7 (i) hadi (vii) imetoa maelekezo juu ya ujenzi na utunzaji wa viwanja vya michezo. Sera imezielekeza Halmashauri kutenga maeneo ya viwanja kila wanapopima makazi ya watu na pia kutumia wadau mbalimbali na raslimali zilizopo katika Halmashauri zao ili kuwajengea wananchi viwanja ili wapate mahali sahihi pa kushiriki shughuli za michezo ili kukuza na kulinda afya zao na pia kupata eneo la kutolea burudani za wazi.

Mheshimiwa Spika, kutokana na Mkakati wa Taifa wa utekelezaji wa Sera ya Maendeleo ya Michezo wa mwaka 2022 mpaka 2032, nitumie nafasi hii kutoa rai kwa uongozi wa Halmashauri ya Hai na Halmashauri zote nchini pamoja nanyi Waheshimiwa Wabunge wote kuendelea kutenga fedha za ujenzi wa viwanja katika viwanja katika bajeti zetu za Halmashauri husika na kuendelea kuwashirikisha wadau mbalimbali wa michezo katika kukamilisha azma hiyo ya kuwa na viwanja na miundombinu bora ya michezo mbalimbali hapa nchini. Ahsante. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali haioni haja ya kuufanya Uwanja wa KIA kutumika kuinua kilimo na kuruhusu ndege za mizigo kutua bila kulipa Landing Fees?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saasisha Elinikiyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hakuna ndege mahsusi za mizigo zenye ratiba maalum zinazotua KIA. Mizigo yote inayopitia KIA hubebwa na ndege za abiria kwenye sehemu ya mizigo. Aidha, kwa sasa idadi ya ndege kubwa za abiria imeongezeka na hivyo kuongeza uwezo wa kubeba mizigo.

Mheshimiwa Spika, Serikali inafanya juhudi mbalimbali kuimarisha biashara ya usafirishaji wa mizigo kwa njia ya anga ikiwemo kununua ndege maalum ya mizigo (Boeing 767 – 300F) ambayo inatarajiwa kuingia nchini kufikia Juni, 2023, kwa lengo la kuhakikisha kwamba biashara hiyo inaimarika. Aidha, ili kuvutia biashara ya mizigo, Serikali ipo tayari kufanya mapitio ya landing fee kwa ndege za mizigo kama ilivyopendekezwa na Mheshimiwa Mbunge. Ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kudhibiti madalali wanaodalalia mazao ya wananchi yakiwa shambani kwa bei wanazozitaka?
WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mpango wa uanzishwaji wa vituo rasmi vya uuzaji na ununuzi wa mazao ya kilimo karibu na maeneo ya uzalishaji ili kumuwezesha mkulima kuuza mazao yake kwa bei ya soko na kuzuia uuzwaji wa mazao shambani. Vilevile Serikali inaendelea na mpango wa ujenzi wa ghala za kuhifadhia mazao katika maeneo ya uzalishaji ili kuwezesha wakulima kuhifadhi na kuuza mazao yao.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafufua Shule za Msingi za Ufundi Wilayani Hai na kurejesha mfumo wa wanafunzi kufanya mitihani na kupewa vyeti?
WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Elinikyo Mafuwe Saashisha, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali iko katika mapitio ya Sera ya Elimu na Mafunzo ya mwaka 2014 na uboreshaji wa Mitaala ya Elimu ili iweze kuwajengea wanafunzi stadi na ujuzi mbalimbali ikiwemo ufundi utakaowawezesha kuhitimu na kuhimili ushindani katika soko la ajira ndani na nje ya nchi. Mara baada ya mitaala tajwa kukamilika ikiwa ni pamoja na manunuzi ya vifaa na mashine mbalimbali za ufundi, Elimu ya Ufundi itatolewa katika Shule za Msingi na Sekondari. Aidha, utaratibu wa kufanya mitihani ya Elimu ya Ufundi na kupata vyeti utaandaliwa kwa kushirikiana na mamlaka husika kama vile Baraza la Taifa la Elimu ya Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi (NACTVET).

Mheshimiwa Spika, pamoja na mapitio ya Sera na Mitaala, Serikali inaendelea kufanya maboresho makubwa katika Chuo cha Ualimu Kleruu pamoja na Chuo cha Ufundi na Mafunzo ya Ufundi Stadi cha Morogoro (MVTCC) kwa kufanya ukarabati wa miundombinu ikiwemo ujenzi wa mabweni ya wanafunzi kwa lengo la kuongeza fursa ya mafunzo kwa Walimu wa masomo ya Ufundi.

Mheshimiwa Spika, pia Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Mbeya kimeanza maandalizi ya utoaji wa mafunzo hayo katika ngazi ya Stashahada katika Elimu ya Ufundi, (Diploma in Technical Education na Postgraduate Diploma in Technical Education). Kwa sasa mitaala ya masomo hayo inafanyiwa kazi na Tume ya Vyuo Vikuu ili kuidhinishwa na kuanza kutumika katika Chuo hicho. Ahsante sana.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufanya utafiti wa sababu za kuyeyuka kwa theluji ya Mlima Kilimanjaro na kukauka kwa vyanzo vya maji?
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, Mkoa wa Kilimanjaro, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Tanzania inayo mipango na mikakati ya kuendelea kufanya utafiti wa sababu za kuyeyuka kwa theluji ya Mlima Kilimanjaro na kukauka kwa vyanzo vya maji. Kupitia Taasisi mbalimbali za ndani ya nchini, zikiwemo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine, na Chuo Kikuu cha Nelson Mandela, vinaendelea kufanya tafiti kuhusu suala hili. Baadhi ya sababu zilizobainika kuchangia hali hiyo ni pamoja na kuongezeka kwa wastani wa joto duniani, shughuli za binadamu zinazoendelea, ukataji wa miti na uchomaji misitu ovyo.

Mheshimiwa Spika, napenda kuchukua fursa hii kuhimiza uongozi na wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro kuongeza jitihada za kutunza mazingira ya mlima huo kwa kudhibiti uchomaji moto ovyo na kuongeza jitihada za kuhifadhi mazingira na kupanda miti.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya kufufua jengo la viwanda vidogo vidogo – Lwosaa?
NAIBU WAZIRI WA UWEKEZAJI, VIWANDA NA BIASHARA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Uwekezaji Viwanda na Biashara napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha tathmini ya jengo hilo na kupata gharama za ukarabati wa kukamilisha ujenzi wa jengo hilo ambazo ni jumla ya shilingi 293,986,850. Pia Serikali kupitia SIDO inaendelea kufuatilia suala la umiliki wa eneo hilo ili kuanza ukarabati na kumalizia ujenzi. Aidha, Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ukarabati na kukamilisha ujenzi wa jengo hilo ili shughuli kusudiwa zianze kufanyika kwa manufaa ya wananchi wa Lwosaa na Taifa kwa ujumla. Nakushukuru.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuleta mbegu mpya za migomba?
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI K.n.y. WAZIRI WA KILIMO alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa niaba ya Waziri wa Kilimo ninaomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha wa 2022/2023 Serikali kupitia Kituo cha Utafiti wa Kilimo cha TARI – Tengeru imefanikiwa kutumia teknolojia ya chupa (Tissue Culture) katika kuzalisha mbegu bora aina ya TARIBAN 1, TARIBAN 2, TARIBAN 3, TARIBAN 4, FHIA 17 na FHIA 23 ambayo ina ukinzani dhidi ya magonjwa (Madoa meusi na Panama (banana wilt) ambayo yamekuwa yakiathiri tija na uzalishaji wa zao la migomba. Uzalishaji wa miche hiyo pia unafanyika kupitia vituo vya utafiti vya TARI – Uyole na TARI – Maruku.

Mheshimiwa Naibu Spika, hadi kufikia tarehe 30 Aprili, 2023 jumla ya miche 30,000 imezalishwa na kusambazwa kwa wakulima katika Mikoa ya Kilimanjaro miche 5,000, Kigoma miche 9,000 na Kagera miche 9,000. Uzalishaji na usambazaji wa miche hiyo unaendelea ili kuwafikia wakulima katika Mikoa ya Morogoro, Mbeya, Arusha na maeneo mengine yenye fursa ya uzalishaji wa zao la migomba ili kuwezesha wakulima kupanda mbegu bora za migomba na hivyo kuongeza tija na kipato cha mkulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika msimu wa mwaka 2023/2024 Serikali kupitia Taasisi ya Utafiti wa Kilimo Tanzania imepanga kushirikiana na maabara binafsi za Crop Bioscience na maua mazuri kuzalisha na kusambaza takribani miche 1,500,000 ya migomba aina ya Grand Nain ambayo itasambazwa kwa wakulima wakiwemo wakulima wa Mkoa wa Kilimanjaro.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kubadilisha utaratibu wa utoaji vibali vya kuvuna miti ili kuhusisha Kamati za Maendeleo za Kata na Vijiji?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, usimamizi na matumizi ya rasilimali za misitu hufanywa kwa mujibu wa Sheria ya Misitu Sura 323 na Kanuni zake za mwaka 2004. Aidha, katika kuhakikisha matumizi endelevu, Serikali kupitia Wizara ya Maliasili na Utalii huandaa mwongozo unaotoa namna ya kutoa vibali na usimamizi wa jumla wa matumizi ya misitu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia utaratibu huo Serikali ilitoa mwongozo mwaka 2017 unaofahamika kama ‘Mwongozo wa Uvunaji Endelevu wa Mazao ya Misitu.’ Mwongozo huo umebainisha wajumbe wanaounda kamati ya uvunaji ngazi ya wilaya chini ya uenyekiti wa Mkuu wa Wilaya.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kubadilisha Mfumo wa Uandaaji Mpango wa Bajeti ili uwe wa zaidi ya miaka mitano?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali unaongozwa na Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025 ambapo katika kutekeleza malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, Serikali iliandaa Mpango Elekezi wa Muda Mrefu wa miaka 15 kuanzia 2011/2012 hadi 2025/2026 uliogawanywa katika vipindi vitatu vya muda wa kati wa miaka mitano ya utekelezaji (Mpango wa Kwanza wa Maendeleo wa Taifa 2011/2012 hadi 2015/2016, Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa 2016/2017 hadi 2020/2021 na Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa 2021/2022 hadi 2025/2026.

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mfumo wa uuandaji wa mpango na bajeti wenye kutoa mwelekeo wa zaidi ya miaka mitano ambapo mpango na bajeti unaoandaliwa kila mwaka ni sehemu ya utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Maendeleo na Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025, ahsante.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi ya Mheshimiwa Rais ya ujenzi wa soko la kisasa la Kwa Sadala?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Halmashauri ya Wilaya ya Hai imeandaa andiko la mradi wa ujenzi wa soko la Kwa Sadala wenye thamani ya shilingi bilioni tisa. Andiko hilo limefanyiwa uchambuzi na Mkoa ambapo mapungufu yaliyojitokeza yamewasilishwa Halmashauri kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, pindi marekebisho hayo, yatakapokamilika na kukidhi vigezo Serikali itatafuta fedha kutoka vyanzo mbalimbali kwa ajili ya kutekeleza mradi huo.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE K.n.y. MHE. JULIANA D. MASABURI aliuliza:-

Je, lini Serikali itakipandisha hadhi Chuo cha Maendeleo ya Jamii Musoma ili kiweze kutoa shahada?
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante na kwa niaba ya Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Didas Masaburi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ili chuo kiweze kufikia hatua ya kutoa elimu kwa ngazi ya shahada, kinatakiwa kiwe na ithibati kamili na kiwe na vigezo stahiki ikiwemo miundombinu ya kutosha kutoa kozi husika, rasilimaliwatu ya kutosha na yenye sifa stahiki na Bodi ya Uendeshaji.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hatua zinazoendelea ili kuboresha mazingira ya chuo kwa ujumla wake, Wizara itaendelea kushirikiana na wadau wa kisekta kufanya tathmini ya kina kuhusu lini kozi hiyo ianze hasa kwa kuzingatia mahitaji halisi ya soko la ajira kwa wahitimu wa shahada, ahsante. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE aliuliza: -

Je, Serikali ipo tayari kufanya utafiti wa madini katika Kata ya KIA Jimbo la Hai?
WAZIRI WA MADINI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Jimbo la Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST) ipo tayari kufanya utafiti wa Jiosayansi katika Wilaya ya Hai. Aidha, GST iko tayari kutoa ushirikiano kwa wadau wa sekta binafsi wenye nia ya kufanya tafiti za madini, kwa kuwapa taarifa za awali kwa kuwa taasisi hii, imefanya utafiti wa awali na kubaini kuwa hadi sasa jiolojia ya Wilaya hiyo inafaa kwa upatikanaji wa mawe ya ujenzi hasa chokaa mfano katika Kata ya Masama Rundugai.