Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Priscus Jacob Tarimo (29 total)

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini pia ningeomba niende mbele zaidi kwa sababu uhalisia unaonesha wanafunzi wanaosoma shule za binafsi hawapati mkopo either wote au kiasi, lakini pia kwa sababu ya umuhimu wa baadhi ya fani kama udaktari na gharama kubwa ya kusomesha watoto kwenye fani hizo, Serikali inaonaje kuwa na mpango wa muda mrefu ili wanafunzi wote wameweze kupata mikopo kwa asilimia mia moja?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kama ilivyotokana na jibu langu la msingi, Serikali inaendelea kupanua wigo wa bajeti katika Bodi yetu ya Mikopo. Kwa hiyo naomba nilichukue suala la Mheshimiwa Mbunge kwa vile kutoka mwaka 2017, Serikali imeweza kuongeza bajeti katika bodi ya mikopo kutoka bilioni 427 mpaka hivi sasa tuna bilioni 460. Kutokana na hivyo basi, wanufaika ni wengi na wanaendelea kuongezeka kutoka wale laki moja katika kipindi cha mwaka 2015 mpaka kufikia laki moja na arobaini mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunapoongeza bajeti hii tuna hakika tunaweza kufanya coverage kubwa ya wanafunzi. Naomba kutoa taarifa katika waombaji wa mwaka huu wale wa mwaka wa kwanza maombi yote yalikuwa 66,000, lakini waliopata jumla karibu walikuwa 55,000. Kwa hiyo tunaendelea kuongeza ule wigo kwa lengo kuhakikisha kwamba wanufaika wanakuwa wengi zaidi.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini pia ningeomba niende mbele zaidi kwa sababu uhalisia unaonesha wanafunzi wanaosoma shule za binafsi hawapati mkopo either wote au kiasi, lakini pia kwa sababu ya umuhimu wa baadhi ya fani kama udaktari na gharama kubwa ya kusomesha watoto kwenye fani hizo, Serikali inaonaje kuwa na mpango wa muda mrefu ili wanafunzi wote wameweze kupata mikopo kwa asilimia mia moja?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kama ilivyotokana na jibu langu la msingi, Serikali inaendelea kupanua wigo wa bajeti katika Bodi yetu ya Mikopo. Kwa hiyo naomba nilichukue suala la Mheshimiwa Mbunge kwa vile kutoka mwaka 2017, Serikali imeweza kuongeza bajeti katika bodi ya mikopo kutoka bilioni 427 mpaka hivi sasa tuna bilioni 460. Kutokana na hivyo basi, wanufaika ni wengi na wanaendelea kuongezeka kutoka wale laki moja katika kipindi cha mwaka 2015 mpaka kufikia laki moja na arobaini mwaka 2021.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunapoongeza bajeti hii tuna hakika tunaweza kufanya coverage kubwa ya wanafunzi. Naomba kutoa taarifa katika waombaji wa mwaka huu wale wa mwaka wa kwanza maombi yote yalikuwa 66,000, lakini waliopata jumla karibu walikuwa 55,000. Kwa hiyo tunaendelea kuongeza ule wigo kwa lengo kuhakikisha kwamba wanufaika wanakuwa wengi zaidi.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Wizara, ninaomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Manispaa ya Moshi ndiyo manispaa ndogo zaidi Tanzania yenye kilometa za mraba 58; na kwa kuwa upanuzi wa makazi na shughuli za kiuchumi ambazo zinasababisha ukuaji wa mji ule zinakwenda kugusa mamlaka za sehemu nyingine ambazo watendaji wa Wilaya ile hawana mamlaka nazo.

Nini nafasi ya Serikali katika kurasimisha maeneo hayo kabla ujenzi holela haujaendelea?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA
MAKAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Manispaa ya Moshi ina eneo dogo, na katika kupanuka kwake inabidi iguse na maeneo mengine ambayo yako nje ya utawala wa Manispaa ya Moshi. Lakini taratibu za Serikali ziko wazi, pale ambapo maeneo ya utawala yanatakiwa kuongezwa ama kupunguzwa, taratibu lazima zifuatwe kupitia Wizara ya TAMISEMI ili kuweza kujua uhalali wa kuweza kuongeza eneo waweze kupata kama wanavyohitaji. Vinginevyo hawawezi kufanya zoezi katika eneo ambalo si la Manispaa, isipokuwa waliopo Moshi DC wanaweza wakafanya zoezi la urasimishaji na kupanga maeneo yao kutokana na sheria inayo…
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Wizara; na kwa kuwa katika kundi la vijana wanakopeshwa vijana wa kiume na wa kike; na kutokana na Katiba yetu tunawatambua kwa umri wa miaka 18 mpaka 35; na kwa kuwa kuna wanaume wengi ambao ndiyo bread winner kwenye familia zao na ni wazalishaji kati ya miaka 36 – 45; na kwa sababu ni suala la kisera: Je, Serikali ipo tayari kuongeza umri angalau mpaka miaka 45 katika kundi hili la vijana ili wanaume waweze kufaidika na mikopo hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA – (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali imeweka utaratibu huu wa mikopo kwa vijana, wanawake na watu wenye ulemavu. Na katika kundi la vijana asilimia kubwa wanaonufaika na mikopo hii ni vijana wa kiume, lakini definition kwa maana ya tafsiri ya vijana kwa mujibu wa taratibu zetu ni wale wenye umri wa miaka 18 hadi 35. Kwa hivyo, kwa maana ya tafsiri hii ya kisheria Serikali bado haijaweka mpango wa kuongeza umri kwa sababu, lengo la mikopo hii ni kwa vijana na kwa maana ya tafsiri ya vijana ni chini ya miaka 35. Kwa hivyo tunachukua wazo lake, lakini kwa sasa sheria hii itaendelea kutekelezwa wakati tunafanya tathmini ya kuona uwezekano wa kuongeza eneo hilo.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, lakini nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali hii ni ya Rufaa ya Mkoa na ukisoma vitabu vya bajeti kwenye mwaka uliokwisha ilikuwa inahudumia wagonjwa karibu 75,000; mwaka huu ambao tunaumalizia wameongezeka wamefikia 96,000 na ni ongezeko la karibu asilimia 13. Lakini pia vitu vya kawaida kabisa kama nyuzi za kushona, kama giving set, vitu vya kawaida kabisa kwa ajili ya huduma ya akinamama havipatikani na ni Hospitali ya Rufaa.

Je, Serikali inatoa commitment gani kuhakikisha vitu hivi vya kawaida kabisa vinapatikana wakati tunasubiri ukamilishaji wa jengo hilo la mama na mtoto?
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. DKT. GODWIN O. MOLLEL): Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Mbunge Priscus Tarimo kwa jinsi ambavyo anafuatilia kwa umakini sio tu hospitali yetu ya Mawenzi, lakini na Hospitali ya Kanda ya Rufaa ya KCMC hasa kwenye maeneo ya miundombinu, lakini kwenye kuwatetea na kufuatilia maslahi ya watumishi wa hospitali zetu hizi zote mbili.

Swali lake ni kwamba ni lini Serikali itahakikisha kwamba vifaa vinapatikana, ametaja nyuzi na vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo huko nyuma mmesikia Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan mwezi wa pili alitoa shilingi bilioni 43 kwa ajili ya vifaa tiba na dawa, lakini mwezi wan ne alitoa shilingi bilioni 80 kwa hiyo, ukijumlisha ni kama shilingi bilioni 123 zimetolewa kwa ajili ya eneo hilo la huduma ya tiba. Kikubwa ni kwamba ndani ya mwezi mmoja vifaa hivyo vitakuwa vimefika kwa sababu vimenunuliwa viwandani na hilo tatizo litakwenda kuisha na hospitali yetu itakuwa na vifaa vyote ambavyo vinahitajika. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyogeza.

Kwa kuwa vigezo vipya vya kufungua maduka vimekuwa vigumu kwa wafanyabiashara wengi, ikiwa ni pamoja na uoga wa kupoteza fedha kama ilivyotokea mwanzo, Serikali ina mpango gani wa kuweka masharti ambayo ni rafiki ili wafanyabiashara wengi zaidi wafungue biashara hizo kwa sababu maeneo ya mpakani/mikoa hii ya mpakani kumeshaanza kuwepo kwa black market ambapo wale wanaobadilisha fedha wanabadilisha kwa bei ya chini sana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; maduka yale yaliyofungwa fedha taslimu zilichukuliwa na baadhi ya wafanyabiashara zilichukuliwa mali zao nyingi ikiwepo hati za viwanja na nyumba, hati za magari kwa maana ya kadi za magari na hawajarejeshewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni nini hatma ya watu hawa ambao wamefungwa mikono na mali zao zimeshikiliwa na Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimo Mbunge wa Moshi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amesema kwamba vigezo vilivyowekwa ni vigumu, lakini bahati mbaya hakuainisha vigezo hivyo ni vipi vigumu; kwasababu imani yangu ni kwamba pengine angetusaidia kutuambia ni kipi kigumu tungeweza kukifanyia kazi. Hata hivyo kwa ujumla vigezo vilivyowekwa mpaka sasa hivi tunadhani tumeviwekwa kwa kuzingatia maslahi ya nchi pamoja na maslahi ya Serikali. Ingawa bado kuna mwanya wa kuweza kuviangalia kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema, lakini kwa uelewa wangu vigezo hivyo kwa kweli si vingi sana. Labda kigezo kimoja ambacho kimekuwa kikilalamikiwa sana ni kigezo cha kiwango cha mtaji kutoka shilingi milioni 300 kuja bilioni moja.

Mheshimiwa Spika, mantiki ya kuweka kigezo hiki ilikuwa ni nia njema tu ya Serikali kuhakikisha kwamba hawa wafanyabiashara wa maduka haya ya kubadilisha fedha wanatumia fedha zao wenyewe kuendesha biashara. Kwasababu wakati ambapo umefanyika utafiti kupitia forensic audit iliyofanywa iligundulika kwamba wengi wafayabiashara wa biashara hizi za kigeni walikuwa wanazungusha fedha isiyokuwa yao, kwa hiyo, hiyo ndio ikawa mantiki ya kuweka kiwango hicho na hivyo nadhani ndiyo malalamiko mengi makubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Mbuge labda pengine angetusaidia kwa wakati wake kuweza kuainisha vigezo. Kama kuna vigezo ambavyo tunaona kwamba vinahitaji kuangaliwa basi tutaviangalia.

Mheshimiwa Spika, lakini swali lake lingine ambalo ameuliza anazungumzia kuhusiana na hatma ya vifaa vilivyochukuliwa. Ni kwamba baada ya hatua ambazo zimechukuliwa kujitokeza wafanyabiashara hawa waliitwa ili kufanya majadiliano na mamlaka husika; na baada ya majadilliano kumalizika walitakiwa wale ambao walipaswa kulipa walipe, wale ambao walitakiwa kwenda kuchukua vifaa vyao waende wakavichukue.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe wito, kama kuna wafanyabiashara ambao bado hawajachukua vifaa vyao na wanastahili kwenda kuvichukua vifaa vyao waende wakachukue vifaa vyao, na hakuna sababu yoyote ambayo Serikali inaweza kukaa na mali ya mtu bila sababu ya msingi. Kwa hiyo niendelee kuwasisistiza kwamba kauli rasmi ya Serikali ni kwamba kama ambavyo majadiliano yalifanyika wakaelezwa wale ambao wanastahili kwenda kuchukua au wanahitaji kuvichukua basi waende wakavichukue. Kama kuna mapungufu yoyote basi tuletewe hizo taarifa ili tuweze kuzifanyika kazi.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri swali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Manispaa ya Moshi imekuwa ikileta orodha ya viwanja ambavyo wamiliki wake hawajaviendeleza kwa muda mrefu:-

Je, ni lini Wizara itaridhia na kufuta viwanja hivyo?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza katika majibu yangu ya msingi, utwaaji wa ardhi yoyote ni jambo la mchakato na utaratibu huo unaanza katika vikao vyenu kule chini katika Halmashauri yenu.

Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Mbunge, waanzishe mchakato huo, walete katika level ya Wizara, tumpelekee Mheshimiwa Rais kwa hatua nyingine zinazotakiwa kufanyika. Ahsante. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lini Serikali itakamilisha upanuzi wa barabara ya Moshi – Arusha kipande kinachoanzia Tengeru - Moshi mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimo, Mbunge wa Moshi kama ifuatavyo: -

Mhesimiwa Mwenyekiti, huu ni mwendelezo wa barabara ambayo ipo kwenye mpango. Tayari tumeshaanza huko Arusha na tunategemea kwa sababu ni barabara muhimu kutoka Arusha kwenda Holili naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ipo kwenye mpango na tunaendelea. Ninaamini katika bajeti inayokuja barabara hii itapata mwendelezo wa kuijenga hatua kwa hatua kadri fedha inavyopatikana. Ahsante. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Ninaomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itapeleka fedha kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya pale Moshi Mjini, kwa sababu ilishapitishwa kwenye bajeti na wengine wameshapata?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo Mbunge, wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mwaka huu wa fedha Serikali imetenga shilingi bilioni 14 kwa ajili ya hospitali za halmashauri 28 katika hamashauri ambazo hazina kabisa hospitali za halmashauri ikiwemo Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Kwa hiyo, nikuhakikishie kwamba ndani ya mwaka huu wa fedha lengo la Serikali ni kuleta fedha hiyo, milioni 500, ili kazi ya ujenzi iweze kuanza. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Wizara yake itaridhia upanuzi wa Mji wa Moshi kufikia kilometa za mraba 142 ukizingatia sasa hivi tuna kilometa za mraba 58 na maombi yako ofisini kwao; na hata damp tumenunua Moshi Vijijini na makaburi yanajaa, tutahitajika tena kununua pia?
NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli maombi ya Mheshimiwa Priscus yalifika katika Ofisi zetu, lakini kama inavyofahamika mwenye mamlaka ya kuongeza maeneo ya kiutawala ni Mheshimiwa Rais. Hivyo, maombi yake tuliyapeleka katika ngazi husika na majibu yatakapokuwa yametolewa tutamjulisha Mheshimiwa Mbunge. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Serikali itafanya upanuzi wa barabara ya Moshi – Arusha kuanzia Tengeru – USA – Moshi Mjini – Himo mpaka Holili?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE):
Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, barabara hii imetengewa fedha kuijenga, kwa maana ya kuikarabati, ikiwa ni pamoja ya kujenga daraja la Mto Karanga. Kwa hiyo, taratibu zinaendelea ili kuanza kuijenga hii barabara ikiwa ni kuikarabati sasa kwa kiwango kikubwa kwa mwaka huu wa fedha. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Je, kuna katazo lolote la watu hawa (wamachinga) kupangwa katika maeneo ya wazi katika halmashauri na maeneo ya taasisi?

Pili; je, Serikali inaweza kutoa ruhusa kwa ajili ya wamachinga, hasa waliokuwa wanauza mananasi, kuweza kujipanga eneo la Railway na wale wa samaki kurudi eneo la Manyema? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, inawajali sana wananchi wake, hasa wafanyabiashara wadogowadogo. Rais ametoa shilingi milioni 10 kwa kila mkoa kwa ajili ya kujengwa ofisi za wafanyabiashara wadogowadogo.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, tayari imeshachora michoro hiyo kwa ajili ya ujenzi huo. Wafanyabiashara hawaruhusiwi kufanya biashara zao katika maeneo ya wazi na ya taasisi. Wafuate maelekezo ya viongozi wao wafanye biashara katika maeneo waliyopangiwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali lake la pili, eneo la wazi la Manyema, Moshi limetengwa kwa ajili ya shughuli za reli. Wafanyabiashara hawaruhusiwi kufanya biashara kwa ajili ya usalama wao, lakini pia kuzuia shughuli za shirika la reli hiyo.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Moshi tayari imeshawatengea wafanyabiashara hao walioondoshwa katika eneo la Reli la Manyema kufanya biashara zao katika maeneo mengine. Ahsante. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Makampuni mbalimbali ya simu yanatoa huduma za mikopo kupitia mitandao na riba zake ziko juu sana: -

Je, Benki Kuu inafanya nini kuhakikisha inasimamia huduma hizi?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Benki Kuu ya Tanzania inapitia maombi yote ambayo yanaletwa na makampuni mbalimbali. Itakapojiridhisha, basi itatoa leseni kwa kampuni yoyote ikizingatia masharti kwamba lazima waambatane au washirikiane na kampuni au taasisi ambayo ipo ndani ya nchi yetu. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Manispaa ya Moshi ilipata shilingi milioni 500; mwaka wa fedha ulipita na mwaka huu wa fedha ilipata shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Wilaya. Hata hivyo mpaka sasa ujenzi huo haujaanza kutokana na kutokuwepo na mawasiliano mazuri kati ya TAMISEMI, Ofisi ya Mwanasheria Mkuu na Wizara ya Fedha. Sasa ni lini ujenzi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikwishatoa maelekezo kwamba fedha za miradi ya maendeleo zikiwemo za ujenzi wa hospitali zikishapelekwa katika Halmashauri ujenzi unatakiwa kuanza mara moja ili kupeleka huduma kwa wananchi. Naomba kutumia fursa hii kumuelekeza Mkurugenzi wa Manispaa ya Moshi kuhakikisha wanaanza ujenzi wa hospitali hiyo mapema iwezekanavyo ili dhamira ya Serikali ya kuwahudumia wananchi iweze kutimia, ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Serikali anayoiongoza kwa kutupatia fedha za kumalizia jengo la mtoto katika Hospitali ya Mkoa wa Kilimanjaro, Hospitali ya Mawenzi. Tangu alipoitembelea Octoba 2021 fedha zimekuwa zikija na fedha za UVIKO zimekuja, na sasa jengo lile linamalizika. Sasa swali langu ni;

Je, ni lini Serikali itaanza mpango wa kuitengeneza master plan ya hospitali ile upya ili kuondoa yale majengo ya zamani na kuweka majengo mapya ya ghorofa yanayoendana na hospitali za kisasa?
NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimwambie Mbunge Rais wetu Daktari Samia Suluhu Hassan alipotembelea pale Hospitali ya Mawenzi yeye aliomba mambo kadhaa na mambo hayo Rais wetu ameshatoa hela. Aliomba bilioni sita ya kumalizia jengo la mama na mtoto na tayari bilioni sita zimekwenda. Pia aliomba CT-Scan, tayari imekwenda, aliomba bilioni 1.3 kwa ajili ya emergency department imeshajengwa na bilioni 1.3 imekwenda, na jana zimekwenda bilioni moja kwa ajili ya kuendeleza kazi ambayo unasema kwamba kubomoa yale majengo ya zamani na kunyanyua mengine ambayo yatafanya ile hospitali iwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna moja tu ambalo tunaenda kutekeleza kabla ya Juni mwaka huu ambalo ulimwomba Mheshimiwa Rais; la ujenzi wa Kiwanda cha kuzalisha gesi tiba, hilo litaenda kutekelezwa kabla ya Juni na kazi itaenda pale vizuri sana. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge nikuhakikishie kazi uliyomwomba Rais inaendelea kufanyika na ahadi amezitekeleza takriban zote. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, kwa kuwa matukio haya yamekuwa yanajitokeza mara kwa mara na inaonekana uwezo wa Wizara kupambana nayo bado ni mdogo.

Je, hawaoni umuhimu wa kurudisha huduma hii ya zimamoto kwa Halmashauri?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu Mkoa kama wa Kilimanjaro una gari moja tu la zimamoto ambalo ni vigumu kuweza kufika mahali kwa muda mfupi. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha angalau tunakuwa na gari la zimamoto kila Wilaya? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kuhusu kurejesha suala hili la zimamoto kwenye local governments, naomba nimkumbushe Mheshimiwa Mbunge kwamba lilikuwa hivyo kabla ya mwaka 2010 ikaonekana uwezo wa Serikali za Mitaa kumudu jukumu hilo ni mdogo sana na ikaelekezwa Serikali Kuu ichukue jukumu hilo na ndio sheria ikabadilishwa Serikali za Mitaa zikarejesha jukumu hilo ngazi ya kitaifa.

Mheshimiwa Spika, sasa tunachoweza kufanya ni kuimarisha na bahati nzuri kupitia bajeti ijayo tuna zaidi ya magari ya zimamoto 12 yatanunuliwa na uokozi yakiwemo magari yenye ngazi, lakini vilevile tumepata mkopo kutoka Austria ambao utasaidia kuimarisha uwezo wetu wa kupata vifaa kwa ajili ya kuzimia moto.

Kwa hiyo, tusikate tamaa tunaendelea kuimarisha jeshi hili bila shaka baadaye litaongeza weledi katika eneo hilo, nashukuru.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Waziri ni lini Serikali itakamilisha mpango wa kupanua Mji wa Moshi na hatimaye kuwa Jiji kama ilivyokuwa kwenye Gazeti la Serikali la tarehe 15 Julai, 2016?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, nashukuru. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, narejea kwenye jibu langu la msingi, kwamba Halmashauri ya Moshi, inahitaji kuleta mapendekezo kwa mujibu wa taratibu zilizoelekezwa na sheria na sisi ofisi ya Rais TAMISEMI, tutafanya tathmini na baadaye kuwasilisha kwa mamlaka husika kwa ajili ya maamuzi husika.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; kwa kuwa nia ni kuleta unafuu kwa wananchi wanaozunguka maeneo hayo; na kwa kuwa halmashauri ndio zinazojua zaidi mahitaji ya watu wale, hatuoni kwamba ni muda sasa tuzipeleke fedha hizo kwenye halmashauri badala ya kutekeleza miradi kama inavyofanyika migodi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa katika Mkoa wa Kilimanjaro suala la uoteshaji miti ni hiari, lakini ukataji miti ni suala ambalo lazima upate kibali na miti hiyo wanatumia kwa ajili ya nishati ya moto. Je, Serikali haioni kutafuta namna nyingine ya kuwapatia nishati mbadala kupitia CSR?
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Moshi Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali ya yote nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuendelea kufatilia hizi CSR katika eneo lake analowakilisha. Katika swali lake ambalo ameuliza Serikali haioni haja kupeleka fedha katika halmashauri. Kwenye jibu langu la msingi nimesema kwamba halmashauri pia zinapata asilimia na pia wananchi wanapata asilimia. Lengo ni kufikisha hii miradi kwa jamii ambao ndio hasa walinzi wa haya maeneo ambayo tunayahifadhi.

Mheshimiwa Spika, jamii ikijisikia kwamba ni sehemu ya uhifadhi sisi kama Serikali tunafarijika kwamba wanaona uthamani wa eneo lile na ni rahisi sasa hata unapowaelezea uhifadhi namna yake ni nini na thamani ya uhifadhi ni nini. Kwa hiyo kupeleka kwenye jamii ni muhimu zaidi kuliko kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili kwamba uoteshaji wa miti Serikali kupitia hifadhi ya TANAPA ilianzisha mradi wa majiko banifu katika eneo linalozunguka Mlima Kilimanjaro. Majiko haya yalikuwa ni fanisi na walienda kufundishwa kaya mbalimbali katika maeneo hayo na pia tumeingia kwenye mpango wa kuanzisha upandaji wa miti katika maeneo yanayozunguka hifadhi hiyo.

Mheshimiwa Spika, upandaji huu ulianza toka mwaka jana na sasa hivi ni endelevu. Hivyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge kwamba mradi huu utatekelezwa ambapo wananchi wengi wanaozunguka maeneo hayo watapata miche ambayo itapandwa katika maeneo ya vijiji nje ya hifadhi ili irahisishe kupata nishati mbadala. Ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Naomba kuiuliza Serikali. Ni lini wataukwamua mchakato wa kuupanua Mji wa Moshi ambao ulishapita ngazi zote alizozitaja ikiwa ni pamoja na kupata GN Na. 19 ya tarehe 15 Julai, 2016?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Priscus Tarimo, Mbunge wa Moshi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilimalizia kusema hapa, kwa sasa kipaumbele cha Serikali kwanza ni kuhakikisha tunakamilisha ujenzi wa miundombinu mbalimbali ya maeneo ambayo yalikuwa yamekwisha megwa kupeleka huduma karibu ya wananchi. Baada ya hapo sasa tutaangalia mchakato huo mwingine wa kuweza kuendeleza maeneo kama ambavyo Mheshimiwa Tarimo amezungumza.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, kwa kuwa hitaji letu ni uhalisia kuliko nadharia, kutokana na uhalisia kwamba hata eneo la dampo sasa tumenunua Moshi Vijijini; na moja ya changamoto ni kwamba barabara inayoelekea kwenye dampo hatuwezi kuikarabai sisi kwa sababu haiwezi kuingia kwenye bajeti ikafanye kazi Moshi Vijijini. Na Moshi Vijijini pia haiko kwenye vipaumbele vyao kwa hiyo inatusababisha sisi tuna operate kwa gharama kubwa sana. Lakini pia inasababisha kwa mfano hospitali ya halmashauri inayojengwa Moshi Mjini inabidi ijengwe kwa ghorofa jambo ambalo ni karibu mara mbili ya gharama za kutengeneza maeneo mengine.

Je, tukiachana na Suala la Jiji ni lini mtakubali tupanue kuendana na GN namba 219 ya tarehe 15, July 2016 ikiwa ni pamoja na kupata maeneo ya makaburi ambayo hatuna?

Swali la pili; yapo maeneo kwenye kata, kwa mfano kata ya Shirimatunda, eneo la Boniti ambalo lilikuwa la viwanda lakini sasa hivi limesharasimishwa kuwa makazi lakini haliwezi kuendelea ili watu wapate hati zao kwa sababu ya kusubiri mchakato huo.

Je, hamuoni kwamba kuna uwezekano wa kutoa upendelea kwa Moshi Mjini kwanza?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa
Spika, nikienda kwenye swali lake la kwanza la Mheshimiwa Tarimo la uhitaji huu ni uhalisia; Serikali inatambua umuhimu wa kutanua mipaka ya Halmashauri ya Manispaa ya Moshi. Lakini kama nilivyosema kwenye majibu yangu ya msingi, kwamba kwa sasa kipaumbele kikubwa ni kuhakikisha tunaimarisha yale maeneo ambayo ni mapya na halmashauri ambazo ni mpya. Ni muda si mrefu halmashauri nyingi zilihamia katika maeneo yao ya utawala, na kwa sasa Serikali hii ya Awamu ya Sita imeweka kipumbele kuhakikisha majengo ya utawala,kuhakikisha huduma za hospitali za Wilaya, kuhakikisha mashule na kadhalika yanajengwa, na hivyo baada ya haya kukamilika Serikali itaanza kutenga bajeti kuhakikisha maeneo mapya ya kiutawala yanatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili, niseme tu kuwa Serikali inalichukua hili ambalo Mheshimiwa Mbunge amelizungumza la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi kupewa upendeleo maalumu kwa sababu tayari GN ilikuwepo. Pale ambapo tutamaliza ukamilishaji wa ujenzi wa miundo mbinu katika halmashauri mpya basi Moshi Mjini Manispaa nayo itapewa kipaumbele.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Kwa kuwa kumekuwa na malalamiko mengi sana kuhusiana na kikokotoo hicho na inaelekea hakuna mpango wa kukirekebisha.

Je, Serikali imejipangaje hata hicho kiasi ambacho kinatolewa, kitolewe kwa wakati?

Swali la pili, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wastaafu sasa hasa wale wanaopata kiasi cha chini, mathalani shilingi 100,000 kwa mwezi, wanaongezewa kiwango hicho cha chini cha pensheni kwa kadri ambavyo mishahara inavyoongezeka?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU (MHE. PASCHAL P. KATAMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Priscus Tarimo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosisitiza kwenye majibu yangu ya msingi kwamba, ndiyo maana tunaendelea kutoa elimu. Suala la kwamba kuna malalamiko, wanufaika wa mifuko hii ya pensheni, katika utoaji wa fedha kulikuwa kuna changamoto ya uwiano wa utoaji wa mafao, pia kulikuwa na changamoto ya uendelevu wa mifuko, tulikuwa na changamoto pia ya mkupuo wa malipo, kwa sasa katika mkupuo wa malipo wanufaika ni asilimia 81 ya wanachama wote, asilimia 19 mafao yao ya kila mwezi yameongezeka.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa katika mkupuo wa malipo, wanufaika ni asilimia 81 ya wanachama wote, na asilimia 19% mafao yao ya kila mwezi yameongezeka. Pia katika kipindi hicho utaweza kuona kwamba katika malipo yale ya kila mwezi, ilikuwa wanaweza kulipwa kwa asilimia 50, lakini sasa yamefikia asilimia 67 ya malipo. Hayo ni maboresho ambayo yametokana na utafiti uliofanyika. Tulifanya actuarial valuation, kwa kuwa mifuko hii ilikuwa na hali mbaya.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka tulikuwa tuna mifuko mingi ya GPF, PSPF, LAPF na NSSF. Mifuko hii kwa ujumla ilikuwa inashindana kwa wanachama wale wale. Utaratibu na maamuzi ya kuiweka pamoja mifuko hii imeleta tija kubwa na sasa mifuko imetoka from loss making trend to profit making venture. Kwa sehemu kubwa utaweza kuona, katika utaratibu huu, ndiyo maana tunaendelea kutoa elimu kwa sababu faida ni nyingi kuliko hasara ambazo zilikuwepo hapo awali.

Mheshimiwa Spika, kwa kweli tutaendelea kutoa elimu. Mheshimiwa Mbunge kama anadhani kuna watu wanalalamika, wote ambao wamekuwa wakifika kwa kutokuelewa utaratibu huu ofisini, wamekuwa wakipewa elimu na wameona faida hii. Namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama anao watu hao, nitashirikiana naye katika kutoa elimu kama jinsi ambavyo mifuko imeendelea kutoa, ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba tunapata ndege za moja kwa moja kutoka Dodoma kwenda Kilimanjaro na Arusha au muda mfupi wa kuunganisha kwa kupitia Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI: Mheshimiwa Spika, tumepokea ushauri wa Mheshimiwa Priscus Tarimo kuhusiana na kuanzisha route inayokwenda Kilimanjaro, nafikiri Serikali itakapokuwa tayari basi ataweza kuarifiwa. (Makofi)
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali, lakini kwanza niseme tu wamejibu upande mmoja, upande wa quality, yaani ubora lakini upande wa bei hawajagusia. Ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu sisi ambao tuko field tumeona kabisa utaratibu huu wa kukagua haufanyi kazi, kwa maana marobota yanayokuja sasa nchini yamejaa nguo chakavu ambazo haziwezi hata kuuzika; je, Serikali haioni namna ya kutafuta utaratibu mwingine wa kuhakikisha wanafanya ukaguzi mzuri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili. Kwa kuwa bei imeonekana bado ni kubwa kutokana na kuwepo kwa madalali, lakini pia ubora unakuwa compromised kutokana na zile nchi nazo zimepigwa na uchumi: Serikali haina mpango mwingine wa kudhibiti biashara hii ili tusiwe dampo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ufanisi wa ukaguzi wa mawakala tuliowapa kazi hiyo kwa mujibu wa maelezo ya Mheshimiwa Mbunge ambaye naamini anawakilisha wafanyabiashara wanaofanya biashara hii ni kwamba ziko chini ya kiwango. Wizara ya Viwanda na Biashara kupitia TBS itafanya uthamini juu ya utendaji wa mawakala waliopewa na kama itathibitika kwamba wanaleta mavazi ambayo yako chini ya kiwango kwa maana ya ubora, lakini na uchakavu hatua zitachukuliwa ikiwa ni pamoja na kuwafutia hizo leseni na kuwatafuta watu wengine wanaoweza kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu bei kubwa ya bidhaa inayotoka kwenye hizo nchi alizozibainisha ambako ndiko wafanyabiashara wetu huchukua mizigo, Serikali kupitia Wizara hii ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji itafanya tathmini na kuangalia masoko mengine kwa maana ya nchi nyingine zinazozalisha bidhaa kama hizo zinazotafutwa na wawekezaji au wafanyabiashara kutoka Tanzania ili wale ambao watakuwa na bei nzuri, basi mwelekeo uwe katika nchi hizo kuliko kuendelea kutumia masoko ya zamani ambayo bei yake ni kubwa, nashukuru.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri; je, Manispaa ya Moshi katika Mradi huu wa TACTIC itaanza lini? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotoa maelezo kwenye majibu yangu ya msingi, hivi sasa wapo katika kuwapata consultants wa ku-design miradi hii na pale watakapopatikana, basi designs zitafanyika na ndipo mradi huu utaanza mwisho wa mwaka wa fedha 2023/24.

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ni lini Barabara ya Tengeru – Holili itaanza kupanuliwa ikiwa ni pamoja na kujenga daraja jipya la Kikavu?

NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, barabara aliyoitaja pamoja na daraja hilo, tayari yapo mazungumzo, na JICA wameshakubali kufadhili ujenzi wa barabara hiyo na daraja hilo la Kikavu ikiwa ni pamoja na barabara kama kilometa 10 katika Mji wa Moshi. Kwa hiyo, sasa hivi suala linaloendelea ni mazungumzo kati ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na JICA ili tuanze kujenga hayo maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge, ahsante. (Makofi)

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa, kuna Halmashauri zenye uwezo wa kuanza mchakato huu kwa kutumia mapato ya ndani kuweza kuweka hii miundombinu. Ni nini commitment ya Serikali kuzisaidia Halmashauri hizi kukamilisha utaratibu huo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili je, kama kuna shule zenye miundombinu na ziko tayari kubadilisha baadhi ya madarasa kuwa ya kidato cha tano na sita. Je, Serikali iko tayari kuruhusu watumie hostel za binafsi wakati wanasubiri kujenga mabweni?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Mwenyekiti, nikijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimo, kwanza kuhusu Halmashauri ambazo zina uwezo wa kujenga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uko wazi kama, Halmashauri ina uwezo wa kujenga miundombinu inayohitajika kwa ajili ya shule yenye mkondo wa Kidato cha Tano na Sita hawakatazwi kujenga miundombinu hiyo lakini ni lazima wafuate taratibu za kukaguliwa na Mkaguzi wa Elimu kwa kuomba usajili wa Kidato cha Tano na Sita kutoka Wizara ya Elimu na kisha shule hii iweze kupandishwa hadhi. Lakini kama wana uwezo wa kujenga hawakatazwi kuweza kujenga lakini wafuate taratibu za usajili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili kuhusu shule ambazo tayari zina miundombinu. Kama kuna shule ambazo tayari zina miundombinu hii hawakatazwi nao kuandika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ili na tuweze kukagua kuona miundombinu iliyopo na kisha kuwasiliana na Wizara ya Elimu kuweza kuomba sasa usajili wa mkondo wa Kidato cha Tano na Sita. Hivyo, niwaombe wenzetu wa Manispaa ya Moshi Mjini kama wanazo shule ambazo tayari wanaziona zinakidhi vigezo basi waombe kwa maandishi kwa Katibu Mkuu wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI na tuweze kutuma timu kwa ajili ukaguzi na kisha kuwasiliana na wenzetu wa Wizara ya Elimu kuweza kuona ni namna gani tunapandisha hadhi shule hizi.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Wizara na taasisi zake zinatekeleza miradi hiyo moja kwa moja badala ya kupitia halmashauri.

Je, hawaoni sasa ni muda muafaka fedha hizo zitengwe zipelekwe halmashauri ili halmashauri itekeleze kwa usawia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwenye Mkoa wa Kilimanjaro tumepitisha sheria kali sana za mazingira zinazozuia kukata miti kwa ajili ya kutunza mandhari ile na hali ya Mlima Kilimanjaro, jambo linaloleta usumbufu kupatikana kwa nishati ya kupikia kwa wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro.

Je, hatuoni sasa kwa Mkoa wa Kilimanjaro ni muda muafaka fedha hiyo ya CSR tuitumie kuwaletea wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro nishati mbadala ya bei nafuu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo ya fedha hizi ni kuhakikisha kwamba zinakwenda moja kwa moja kwenye community, kwa maana ya kwamba kwenye jamii. Hatuna shida na halmashauri lakini tumeona fedha hizi bora ziende moja kwa moja kutoka kwenye taasisi husika kwenda kwenye jamiii moja kwa moja kwa sababu kwanza tumeona jamii iweze kujua mchango wa uhifadhi na vipi wanaweza kunufaika na maeneo yale yaliyohifadhiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili tumeona kwamba, miradi mingi imekuwa inasuasua, sasa tukaona tukizipeleka fedha moja kwa moja, miradi hii itapata kumalizika kwa haraka na jamii iweze kunufaika. Kikubwa zaidi tumeona miradi ambayo inahitajika ndiyo iende kwa jamii. Kwa hiyo kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba wazo lake sawa tunaweza kulichukua tukaona namna ya kulifanyia kazi, lakini kwa sasa tumeona bora fedha moja kwa moja ziende kwa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine nimwambie kwamba, fedha hizi ziko kwa ajili ya miradi mbalimbali ikiwemo maji, umeme, zahanati na hata shule, lakini vile vile tu kwa kuwa sasa suala la nishati mbadala kwa sasa ni ajenda ya kitaifa, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili alilolishauri tunalichukua, tunakwenda kulifanyia kazi ili tuone namna ambavyo tunaweza tukachota fedha kutoka kwenye fungu hili na kuweza kushughulika na masuala ya nishati mbadala kwa sababu ndio ajenda ya Kitaifa, nakushukuru.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali kuhusiana na eneo hili, lakini ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mkakati wa Serikali umejikita kwenye wafugaji wapya wanatoka vyuoni. Ni nini mpango wa kuwawezesha wafugaji hawa wa sasa ambao wengi wanafuga kienyeji?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; upande wa nyama ya kuku kumekuwa na tatizo la vifaranga mara nyingi. Nini mpango wa Serikali kuhakikisha vifaranga vinapatikana ndani vyenye ubora ambao nyama yake inaweza pia kuuzwa nje? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Priscus Jacob Tarimo, Mbunge wa Jimbo la Moshi Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia tasnia hii ya nyama nchini kwa umakini mkubwa. Nimwondoe shaka tu kabisa kwamba mipango ya Serikali siyo kwa vijana wanaotoka vyuoni, ama vijana wa kisasa pekee, ni pamoja na wale ambao wamezoea kufuga kwa mifumo ya kiasili. Kwa hiyo, mipango yetu inajumuisha makundi yote mawili na tunaendelea kufanya hivyo ili kuhakikisha kwamba tunaboresha mbari za mifugo kwa wafugaji wote nchini.

Mheshimiwa Spika, kuhusu upatikanaji wa vifaranga, ndiyo moja ya mikakati ambayo sisi kama Wizara ya Mifugo na Uvuvi tunayo sasa hivi kuhakikisha tunaongeza uzalishaji ili vifaranga vipatikane kwa wingi na tuwasaidie wafugaji wetu, hususan wa kuku, na mifugo mingine, ili tuweze kuuza nje ya nchi kwa wingi mkubwa, ahsante.
MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba kumuuliza Mheshimiwa Waziri, ni lini Barabara ya Moshi – Arusha hasa kipande cha pale Moshi Mjini itapanuliwa ukilinganisha kwamba tayari Mikataba ilishasainiwa?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ni kweli kwamba barabara hii inapanuliwa kutoka Arusha kwenda Moshi ikiwa ni pamoja ya lile Daraja la Kikafu. Hii barabara ambayo ameisema, tunasaidiana na wenzetu wa JICA. Ziko taratibu ambazo zikishakamilika, basi barabara hii itaanza kujengwa, lakini iko mbioni kuanza kujengwa. Ahsante.