Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Mrisho Mashaka Gambo (26 total)

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli imefanya kazi nzuri ya kujenga barabara kwenye Jiji la Arusha na hasa ukizingatia kwamba, barabara ya mzunguko ya bypass ambayo imesaidia sana kwa watalii na wananchi wa Jiji la Arusha, lakini bado kuna kipande cha Kata ya Moshono ambacho kinatoka eneo la kona ya Kiseliani kuunganisha barabara ya bypass maarufu kama barabara ya T Packers Osunyai kama kilometa saba. Je, Wizara ya Ujenzi haioni sasa ni wakati sahihi wa kumalizia kipande hiki ili kupunguza msongamano na kuweka mazingira mazuri zaidi ya utalii pamoja na wananchi wa Kata ya Moshono?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye ukurasa wa 77 barabara za bypass kwa ajili ya kupunguza msongamano zimeainishwa zikiwemo Miji ya Dar-Es-Salaam, Mbeya na Arusha ni kati ya miji ambayo zitanufaika na barabara hizi za mizunguko kwa ajili ya kupunguza misongamano. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha kwamba, barabara hii aliyoitaja ni moja ya barabara ambazo zitatekelezwa katika kipindi hiki tutakachoanza bajeti katika kipindi hiki cha miaka mitano. Ahsante. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, naomba niweke wazi tu kwanza kwamba sijaridhika na majibu ya Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake sekta ya utalii kwa Mkoa wa Arusha na nchi nzima imeathirika sana. Wananchi wengi sana wamekosa ajira, madereva wamekosa ajira kwa sababu magari hayatembei kutokana na uchache wa watalii, guides wamekosa ajira, wafanyakazi wa mahoteli wamepunguzwa kwenye maeneo yao, magari ambayo yangetembea, yangeweka mafuta shell zingeweza kufanya biashara zao.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia kwenye ukanda wa Afrika Mashariki, karibu nchi nyingi zimeweza kupunguza tozo kipindi hiki. Mfano, Kenya, Nairobi National Park wamepunguza tozo kutoka Dola 43,000 mpaka 35,000. Ukienda Rwanda kwenye masuala ya gorilla wamepunguza kutoka Dola 1,500 mpaka Dola 500. Ukienda Uganda kwenye masuala pia ya gorilla wamepunguza kutoka Dola 700 mpaka 500. Naomba Wizara ya Maliasili na Utalii iangalie athari za ugonjwa wa Corona kwenye masuala ya ajira na masuala mengine.

Mheshimiwa Spika, swali langu la nyongeza, Wizara ya Maliasili na Utalii ina mpango gani wa kuipa ahueni sekta ya utalii ili kuweza kunusuru changamoto kubwa ya ajira ambayo imewaathiri wananchi wa Mkoa wa Arusha pamoja na Tanzania kwa ujumla?
WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo Mheshimiwa Gambo ametoa takwimu, wenzetu wamepunguza kutoka Dola 1,500 mpaka 1,000, kutoka Dola 700 mpaka 500; hizo ndiyo takwimu zake. Viwango vya kuingia katika hifadhi zetu bado viko chini sana ukilinganisha na ubora wa hifadhi tulizonazo. Ukisema Serengeti hulinganishi na hifadhi yoyote iliyoko katika Afrika Mashariki; kule Rwanda unaona gorilla tu. Serengeti is a jewel, bado ni Dola 60. Kwa hiyo, viwango bado viko chini sana. Nilitaka kwanza hilo niliweke sawa.

Mheshimiwa Spika, la pili, Serikali inatoa tahafifu gani hasa kwa kipindi hiki? Wizara imegawa suala la utalii katika misimu miwili; high season na low season. Ongezeko hilo ambalo tunalisema litagusa kwenye high season tu; low season bado rates zitabaki pale pale.

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa nini? Katika high season, sehemu kama Ngorongoro kwa siku moja yanaingia magari 400 ambayo yanaathari kubwa kiikolojia wakati kwenye low season yanaingia magari 70. Tunataka tu-balance sasa, hawa wafanyabiashara wetu ambao tutawapa tahafifu, waende sasa kwenye low season ili tutunze pia na ikolojia iliyopo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, AJIRA, KAZI, VIJANA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Spika, pamoja na kuunga mkono majibu mazuri yaliyotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini swali la msingi na maswali ya nyongeza yamegusa pia sekta ya ajira katika sekta hiyo ya maliasili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuliambia Bunge lako Tukufu, wakati wa Covid, hata sasa na hata baadaye, kama kunatokea tatizo lolote linalohusiana na suala la wafanyakazi, tunaomba wafanyakazi, waajiri watumie platform yao ambayo ni ya dhana ya utatu ambayo tumekuwa tukiitumia mara nyingi kuamsha mijadala na kutafuta solution katika mazingira ya mawanda hayo ya sekta ya kazi, ajira na Serikali. Kwa hiyo, nawashauri watumie platform hiyo.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, Mkoani Arusha kuna shule ya St. Jude, ni shule ambayo inasomesha watoto wenye mazingira magumu na kwa kupitia misaada ya watu mbalimbali huko duniani. Siku za karibuni TRA imeenda kwenye account ya shule hiyo imechukua fedha na kusababisha shule hiyo kupata misukosuko na kufungwa kiasi ambacho watoto wenye mazingira magumu wamekosa nafasi ya kwenda kusoma pamoja. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa ahueni kwa shule hii ili suala la elimu ambayo ni kipaumbele chetu liweze kupewa mstari wa mbele?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama alivyobainisha uwepo wa shule hiyo na changamoto zilizotokea kuhusiana na wenzetu wa TRA, suala hili naomba tulichukue twende tukalifanyie kazi na badaye tutaweza kutoa majibu muafaka kwa Mheshimiwa Mbunge na Mkoa wa Arusha kwa ujumla. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa changamoto ya umeme wa Jimbo la Handeni inafanana kabisa na Jimbo la Arusha Mjini, napenda kuuliza maswali ya nyongeza yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba Jiji la Arusha ni jiji la kitalii, lakini bado kuna kata ambazo zinachangamoto kubwa sana ya umeme Kata kama za Telati, Kata ya Olasiti, Olmoti, Moshono, Mulieti kule maeneo ya Losoito, Sokoni 1 na Sinoni. Ningependa kufahamu, je, Wizara ina mpango gani kupitia Mradi wa Peri-urban ili kuhakikisha kwamba wananchi hawa ambao wapo kwenye Jiji la Kimataifa, Jiji la Utalii wanaondokana na changamoto ya umeme katika jimbo letu?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili….

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa moja tu, hilo ni la nyongeza.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gambo, Mbunge wa Arusha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inapeleka umeme katika maeneo mbalimbali kwa programmes tofauti. Ziko awamu za REA ambazo zimeendelea, ziko programme ya densification, lakini ipo programu peri-urban ambayo inapeleka umeme kwenye maeneo ambayo yana asili ya ukijiji lakini yako mjini. Mkoa wa Arusha tayari umeshanufaika na awamu ya kwanza ya densification, peri-urban kupeleka umeme katika baadhi ya maeneo na iko awamu ya pili ya peri-urban ambayo itakuja, inaanza mwezi wa Saba.

Katika maeneo ambayo hayajapata Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Mwanza na Tanga yatapelekewa umeme katika Mradi huo wa pili wa peri-urban. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba awamu hiyo ya pili ikianza basi na yeye maeneo yake yatapatiwa umeme katika awamu hiyo.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri na Waziri lakini tumeona kwamba pamoja na faini ya bodaboda kuwa kubwa, lakini bado matukio ya uhalifu yameongezeka kwa hiyo ni ishara kwamba faini haiwezi kuzuia uhalifu, lakini ukiangalia pia katika utaratibu wa kawaida sasa hivi tuna changamoto kubwa ya ajira katika nchi yetu na Serikali yetu imeahidi kutoa ajira milioni nane na miongoni mwa watu ambao wanajiajiri sehemu yao ni bodaboda.

Mheshimiwa Spika, nadhani ni vizuri sasa Wizara ya Mambo ya Ndani ikaleta utaratibu hapa ili tuweze kupitia upya mchakato wa faini hizi kwa sababu tunafahamu mtu leo ukiua una adhabu yake, lakini pia leo mtu ukiiba kuku una adhabu yake, haiwezekani gari ambalo ni milioni mia tatu faini yake elfu thelathini na pikipiki ya milioni mbili faini yake elfu thelathini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hapa tunasema elfu thelathini kama ni kosa ni moja, bodaboda anaweza kupigwa makosa manne kwa siku akalipa laki na ishirini na pikipiki ile sio ya kwake, inabidi pia apekeleke hela kwa mwenye pikipiki na yeye pia aweze ku-survive. Nadhani Serikali iwaangalie kwa jicho la huruma watu hawa wa bodaboda ili changamoto iweze kuondoka.

Mheshimiwa Spika, swali langu katika eneo hili tumeona watu wa traffic wamekuwa kwa kiwango kikubwa wanawakamata sana bodaboda pamoja na watu wa bajaji. Je, Wizara ya Mambo ya Ndani ina mpango gani wa kutoa maelekezo mahususi kwa watu wa traffic ili sio kila kosa analokamatwa nalo mtu lazima apigwe faini waweze kutoa onyo pamoja na utaratibu mwingine?

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. (Makofi)
WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kumekuwa kukijitokeza baadhi ya askari wetu kutokuwa waungwana. Unajua shughuli hizi huwezi ukazi-control kwa sheria per se a hundred percent. Kwa hiyo, hekima, busara na hasa unapokuwa mtumishi wa Umma unayewatumikia watu lazima utumie hekima na busara. Enforcement a hundred percent na yenyewe huwa kidogo ina shida. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge, lakini pia na Waheshimiwa Wabunge mtusaidie, baadhi ya vijana wetu wanafanya kusudi na ninyi wenyewe mashuhuda, mnaendeshewa vibaya sana bodaboda hata hapa mjini, tukiacha hii hali na yenyewe ni shida pia. Mimi niseme tu, sote tutekeleze wajibu wetu na kwa upande wa askari polisi, hasa wa usalama barabarani wajitahidi kuwa wanatumia busara katika kuhakikisha kwamba wanasimamia sheria siyo kukomoa.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, napenda nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu hayo, lakini ujenzi wa stendi hii ulitakiwa uanze toka mwaka 2010/2011 ambapo Serikali iliweza kuzuia maeneo ya wananchi wa Kata za Moshono na Kata za Olasiti na maeneo hayo yaliwekwa mpaka kwenye master plan ya Jiji la Arusha. Sasa hivi Serikali imefanya maamuzi ya kwenda kujenga stendi kwenye eneo lingine la Bondeni City.

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yangu ya nyongeza, napenda kufahamu kwanza, je, sasa Serikali ina mpango gani na yale maeneo ya Olasiti na Moshono ambayo yalitengwa maalum kwa ajili ya kujenga stendi na yameishingia kwenye master plan? Je, Serikali sasa hivi inawaruhusu wananchi wale waende wakayaendeleze maeneo yao? Je, wako tayari kupabilisha master plan au Serikali inao mpango wa kulipa fidia?

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho wa siku wananchi wale walitarajia kwamba Serikali ingeweka shughuli yoyote ya kiuchumi pale, hata kama sio stendi, pengine soko au shughuli yoyote, ingesaidia shughuli za kiuchumi za watu wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la nyongeza …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mrisho Gambo ushauliza maswali matatu tayari katika swali lako la kwanza la nyongeza na maswali yanayoruhusiwa ni mawili. Mheshimiwa Naibu Waziri, majibu.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunielewa.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali kwa dhamira ile ya kuhakikisha inaboresha miundombinu ya vitega uchumi kwa maana ya miradi ya kimkakati katika Jiji la Arusha, ilitenga maeneo haya na mradi huu ulitarajiwa kuanza mwaka 2010/2011. Yale maeneo ambayo yalitengwa awali, ni yale ambayo wananchi waliahidiwa kwamba watafidiwa lakini pia ili kitega uchumi kiweze kujengwa eneo lile.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna sababu kadhaa ambazo zilifanya Halmashauri ya Jiji la Arusha lakini na Serikali kuona ni vema sasa eneo la Bondeni City ambalo ni kubwa na linaweza likasaidia zaidi kwa maana ya geographical location yake kuwa na stendi ya kisasa ambayo itasaidia zaidi kuboresa mapato lakini pia huduma kwa wananchi wa Arusha. Naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo kwamba nalichukua jambo hili twende tukalifanyie tathmini zaidi, tuweze kuona sababu ambazo zimetupelekea kuhamisha kwenda sehemu nyingine lakini tuweze kuona nini kitafanyika sasa katika lile eneo ambalo mara ya kwanza lilikuwa limedhamiriwa kujenga stendi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sehemu ya pili naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama nilivyotangulia kusema Serikali inadhamiria kujenga miradi hii ya kimkakati yakiwemo haya masoko kisasa. Kwanza kuboresha huduma kwa wananchi, lakini pili kuwezesha halmshauri kupata mapato katika vyanzo vyake vya ndani. Baada ya tathmini hiyo na baada ya kumpata Mkandarasi Mshauri tutahakikisha kwamba tunakwenda kuanza ujenzi wa soko hilo la kisasa katika Jiji la Arusha.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza sijaridhika kabisa na majibu yaliyotolewa na Serikali kwa sababu wakati anaongea maneno haya Kiwanda cha TPI tayari mwekezaji aliyeko pale ameshauza ekari tano kwa 1.3 billion kwa mtu mwingine na ukizingatia Serikali ina share ya asilimia 30 kwenye kiwanda hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza, tunafahamu kwamba Serikali ilipeleka kiasi cha dola milioni 10 kwenye Kiwanda cha General Tire. Ningeomba nipate majibu leo hapa fedha hizo zimefanya kazi gani na zimeendeleza nini katika kiwanda hicho ili kiweze kutoa ajira na fursa kwa watu wa Arusha na Watanzania?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani pia wa kufufua kiwanda chetu cha TPI ili tuweze kuongeza dawa, lakini pia na kuongeza ajira kwa watu wetu wa Arusha na nchi nzima ya Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kuhusu Kiwanda cha TPI, asilimia 30 ya kiwanda hicho Serikali ina own share. Kwa hiyo, Serikali iko katika hatua za kutafuta mwekezaji ambaye atawekeza kwa ubia na Serikali, ili kiweze kufufuliwa. Kama Mheshimiwa Mbunge ana mwekezaji yeyote na Bunge hili na Watanzania wote, Kiwanda cha TPI kiko open kwa kumpa mwekezaji kwa kiwango cha asilimia 70 ili kiweze kufunguliwa. Ni dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba kiwanda hicho kinafunguliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu Kiwanda cha General Tire, ni kweli Serikali iliweka fedha na ni kweli kwamba mwekezaji aliyekuwa amewekeza eneo lile na aliyekuwa amepewa ownership ya kuki-run kiwanda kile alikabidhiwa fedha na tathmini ya awali ilionesha kwamba fedha zile hazikuweza kufikia malengo yaliyokuwa yametarajiwa. Kwa hiyo, Serikali hatua iliyochukua ni kuhakikisha kwamba kwanza inakirudisha mkononi mwake na kukikabidhi Shirika la NDC kukitafutia mwekezaji mwingine. Yule bwana aliyekuwa amepewa majority shareholder share zake zilirudishwa Serikalini. Kwa hiyo, ni dhamira ya Serikali kuona kwamba Kiwanda cha General Tyre kinafanya kazi ili kufikia lengo la Serikali kwa ajili ya kuwekeza katika eneo hilo.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba Mheshimiwa Waziri hafahamu kwamba hii ni changamoto kubwa sana kwa Jiji la Arusha na inaathiri karibuni Kata 15 Kata ya Ulolieni, Kata ya Balaha, Kata ya Sekei, Kata ya Kimandolu, Sakina, Kaloleni, Revolosi, Sombetini Osunyai, Unga Limited, Yalelai, Daraja Mbili, Mulieti, Sokonwali na Sinoni. Unaona zaidi ya nusu ya kata zote zina changamoto hii.

Mheshimiwa Spika, kwanza nilikuwa naomba kufahamu ni wadau gani walioshirikishwa ikiwa Ofisi ya Mbunge haijashirikishwa, nimeongea na watu wa TARURA hawajashirikishwa, lakini na madiwani pia wa kata zinazohusika pia awajashirikishwa; kwanza ningependa kufahamu ni wadau gani ambao wameshirikishwa kwenye hii study na kwenye solution ya hili jambo?

Mheshimiwa Spika, lakini ya pili nilikuwa naomba kwa uongozi wako kwa sababu jambo hili linahusisha Wizara mbili; Wizara ya Uchukuzi pamoja na wizara ya TAMISEMI; je, Waziri haoni haja kwamba wizara hizi mbili tukafanya kikao pale Jijini Arusha, kwa kushirikisha Mkuu wa Mkoa pamoja na Mkuu wa Wilaya ili mwisho wa siku tutafute solution ya kudumu kwa wananchi wetu wa Jimbo la Arusha Mjini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu langu la msingi ni kwamba baada ya kupata hii changamoto ambayo mafuriko yanasababishwa na maji kutoka mlimani na Mheshimiwa Mbunge amekuwa analifuatilia sana, Serikali imeamua kufanya study kuona namna ya kuondosha hili tatizo.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwenye study hii baada ya kukamilika, itakapokuwa taarifa imepatikana hatutaanza kutekeleza mradi hapo ndipo tutakaposhirikisha wadau kulingana na taarifa za study zitakavyokuwa zimeonyesha kwamba sasa tunategemea kufanya hiki na hiki.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya tafiti hiyo kukamilika wadau hawa watashirikishwa kabla ya kuanza kutekeleza huo mpango ambao utakuwa sasa umebainika kutokana na study hiyo, lakini nikubaliane na Mheshimiwa Mbunge kwamba sisi tulipojenga barabara hii ya TANROADS barabara nyingi zinazoathirika na wananchi wanaoathirika ni wa Wizara sana wanaoshughulikiwa na TARURA na TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge sisi kama Serikali tunafanya kazi kama timu tutaongea na TAMISEMI na si TAMISEMI tu tu pengine hata ofisi za mazingira na hata watu wa kilimo ambao pengine huko wanasababisha miundombinu yetu kuharibika. Kwa hiyo, nimuhakikishie Mbunge kwamba kama Serikali tunafanya pamoja kuhakikisha changamoto hii tunaiondoa, ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa sababu kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa wafanyabiashara wa bureau, kwamba assessment ambazo zimefanyika hazikufanya na competent authority kwa sababu zilifanya na task force badala ya kufanywa na TRA kama wahusika.

Je, Wizara ya Fedha haioni sasa kwamba wakati umefika kwa TRA kwenda kupitia upya zile assessment ili yale makadirio yaani makadirio ambayo yapo kwa mujibu wa sheria?
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Gambo Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ninatambua Mheshimiwa Mrisho Gambo ni miongoni mwa watu ambao wananchi wa jimboni kwake wameathirika na jambo hili; na ikiwa kama Mbunge anawajibu anapopelekewa malalamiko na wananchi hapa ndipo sehemu yake pa kuyasemea.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo nimhakikishie Mheshimiwa Gambo kwamba assessment hii imefanywa na TRA kupitia Kitengo kile cha Investigation, kwa hiyo ni assessment ambayo imefanywa kwa mujibu wa taratibu na sheria na mamlaka sahihi kabisa ambayo inapaswa kufanya assessment.

Mheshimiwa Spika, lakini kama nilivyosema mwanzo, kwamba tuna utaratibu ambao iwapo mtu hajaridhika na assessment yote kuna utaratibu wa kufuata ili kuweza kuhakikisha kwamba anakata rufaa katika ngazi mbalimbali na kuangalia kama kuna uwezekano wa kuweza kui-review assessment yake ukafanyika hivyo.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie tu kwamba jambo hili lilisimamiwa na TRA wenyewe katika eneo la investigation.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa changamoto iliyopo Jimbo la Nsimbo linashabihiana kabisa na changamoto ya Jiji la Kitalii la Arusha; tunazo kata ambazo zilikuwa zamani Wilaya ya Arumeru kabla hatujawa jiji Kata kama ya Olmoti ambayo ina mitaa ya Nafco na Milongoine, Kata ya Terrat ambayo ina mitaa ya Ulepolosi, Masikilia na Engavunet na Kata ya Olasiti ambayo ina mtaa wa Oloesho bado zina changamoto kubwa ya mawasiliano ya simu.

Je, ni lini Serikali itapeleka mawasiliano ya simu kwenye kata na mitaa hiyo ambayo nimeitaja?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nimpongeze Mheshimiwa Mrisho Gambo kwa kazi nzuri anayoifanya katika Jimbo lake la Arusha.

Mheshimiwa Spika, nimeshafika Arusha, na maeneo ambayo ameyataja nayatambua kweli kabisa yana changamoto hiyo. Tayari tumeshaelekeza wataalamu wetu; kwa sababu changamoto ya Arusha si ujenzi wa mnara isipokuwa ni kuongeza nguvu katika minara iliyopo ili iweze kuhudumia wakazi wa Arusha kwa sababu wamekuwa wakiongezeka kwa kasi kubwa hivyo basi minara iliyokuwepo ilikuwa imeshazidiwa nguvu. Tayari wataalamu wetu wameshaanza kufanya kazi na pindi kazi hii itakapokamilika basi changamoto hii itakuwa imeweza kutatuliwa. Ahsante sana.
MHE. MRISHO S. GAMBO: Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba, Wenyeviti wa Serikali za Vijiji ndio msingi wa Serikali za Mitaa katika nchi yetu, na kwamba, maelekezo mengi ya Serikali kutoka ngazi ya TAMISEMI, mikoa, wilaya na halmashauri yanapelekwa ngazi za chini na wao ndio wanazisimamia.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu, Jiji letu la Arusha limeongoza kwa mapato kwenye hii robo ya kwanza. Na ukizingatia kwamba, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2021/ 2022 tulitenga fedha kwa ajili ya kulipa shilingi elfu 50 kwa kila Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa na bado halmashauri yetu haifanyi hivyo. Je, ni nini kauli ya Serikali kwa Halmashauri ya Jiji la Arusha kuhusiana na changamoto hii ambayo inawakumba Wenyeviti wa halmashauri?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; ukizingatia kwamba, uchaguzi wa Serikali za Mitaa ulifanyika mwaka 2019 na mpaka sasa Wenyeviti wa Serikali za mitaa hawajapatiwa semina, hawapewi stationaries zozote, hawajapewa vitambulisho na hata bendera kwenye maeneo yao pia hazijapatikana na hasa ukizingatia pia hawana hata ofisi. Inabidi wachangishe kwa watu waende wakaombe hela kwa wadau, ili mwisho wa siku waweze kulipia ofisi.

Mheshimiwa Spika, hatuoni kwa kufanya namna hiyo tunawaweka kwanye mazingira ya rushwa Wenyeviti wa Serikali za Mitaa? Je, nini kauli ya Serikali kwenye kutoa heshima kwenye ofisi za Serikali za mitaa?
NAIBU WAZIRI OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA, SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE):
Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, viongozi hawa Wenyeviti wa Vijiji, Mitaa na Vitongoji wanafanya kazi kubwa sana katika kusukuma maendeleo ya nchi yetu. Na ndio maana katika jibu la msingi nimeeleza namna ambavyo Serikali imeendelea kutathmini na kuweka njia bora zaidi ya kuhakikisha tunawawezesha Wenyeviti wa Vijiji na Vitongoji kupata posho zao kila mwezi, lakini kwa sababu halmashauri zetu hazijawa na uwezo wa kutosha tunaendelea kuona namna gani tutaboresha mfumo huu, ili waweze kupata posho hizo.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali ilitoa mwongozo kwamba, kila halmashauri itenge fedha kulingana na uwezo wa mapato yake na iweze kuwalipa posho hizo Wenyeviti wa Mitaa.

Kwa hiyo, naomba nitoe maelekezo kwa Halmashauri ya Arusha na halmashauri nyingi zote nchini, zile ambazo zimetenga bajeti na zina uwezo wa kukusanya fedha hizo ziendelee kuwalipa Wenyeviti wa Mitaa na Vijiji kwa kadiri ya bajeti ambazo wamezitenga.

Mheshimiwa Spika, lakini pili, Serikali imeendelea kutoa fedha ambazo ni fidia ya vyanzo vilivyofutwa (GPG), kwa maana ya asilimia 20 kwa ajili ya shughuli za uendeshaji wa ofisi za vijiji na mitaa. Utaratibu huu unaendelea ili kuwezesha kuweza kununua shajara, lakini na matumizi mengine ya kila siku. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Jiji la Arusha linakua kwa kasi sana na kusababisha misongamano mbalimbali, kwa hiyo napenda kufahamu; je, ni lini Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi itaanza rasmi ujenzi wa barabara ya lami ya kutoka pale Kiserian (Moshono) kuunga na bypass na ile ya Ngaramtoni kwenda mpaka Mianzini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ina mpango wa kujenga hiyo barabara ya kuanzia Moshono kwenda bypass na tayari tumeshaanza, labda ni kuikamilisha tu. Kwa hiyo Serikali bado itaendelea kuijenga hiyo barabara kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, kwa barabara ya pili aliyoitaja ya kuanzia Mianzini kwenda Ngaramtoni yenye urefu wa kilometa 18, ninavyoongea hapa ipo kwenye hatua za manunuzi kuanza kuijenga yote kilometa 18 kwa kiwango cha lami. Ahsante. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa gharama za maisha kwa wananchi wote bila kujali kama wanafanya kazi sekta binafsi au sekta za umma ni zilezile gharama kama mchele, unga na gharama nyingine.

Je, Serikali ina mpango gani ya kuhakikisha kwamba mishahara kwenye sekta binafsi na yenyewe inapanda inakuwa angalau shilingi 370,000 kama ilivyo kwa sekta ya umma? Kwa sababu sasa hivi maeneo mengi ni shilingi 100,000 kuendelea kidogo.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, amesema kwamba wanategemea kutoa mwongozo wa kupandisha mishahara kwa sekta binafsi mwezi Novemba; je, watakapotoa miongozo na mishahara itakapopanda, wakati wengine wa Serikali tayari wameshapandishiwa mishahara toka tarehe 1 Julai; je, mwongozo huo pia utalipa na malimbikizo kwa muda ambao wenzao wameshaanza kulipwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, AJIRA, VIJANA NA WENYE ULEMAVU): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu la nyongeza la Mbunge wa Arusha, Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali lake la kwanza niseme tu kwamba katika mishahara hii ya watumishi wa umma na wale wa sekta binafsi kuna utofauti mkubwa. Katika sekta binafsi tunazo kada tofauti tofauti, wapo wafanyakazi wa mashambani, wapo wa viwandani, wapo ambao ni makampuni binafsi, wapo waliojiajiri wenyewe na ambao wameweza kuajiri watu wachache. Kwa hiyo, uki- standardize na ukawa na standard level ya mishahara kwa kima cha chini inaweza ikaleta ugumu sana tumefanya study kuna best practice katika nchi nyingi ambazo tumeona kwamba huwezi uka-standardize kila mmoja na ndiyo maana bodi inaundwa ili ikafanye utafiti katika kuangalia uhalisia wa hali ya uchumi, lakini pia kazi zinazofanyika katika kila eneo ili iweze kuweza kupanga kulingana na category walizonazo hao wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, wafanyakazi wa viwandani wana category yao, lakini pia na wale wa mashambani na maeneo mengine kulingana na uhalisia wa uchumi wa nchi husika. Kwa hiyo, tumelifanya hilo utafiti katika best practice ya nchi zaidi ya saba Mheshimiwa Mbunge. Kwa hiyo, niña imani kwamba bodi ya kima chini italeta ushauri ambao ni sahihi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, ndiyo mwenye dhamana ya kuamua kwamba hapo kuna haki? Kwa sababu tunachopaswa kuangalia ni zile kazi za staha lakini atumishi aweze kulipwa mshahara wake ambao unafanana na hali halisia ya uchumi.

Mheshimiwa Spika, swali lake la pili, ameuliza kuhusu mishahara hii kwamba kwa upande wa Serikali tayari tumeshatangaza mabadiliko ya mishahara. Kwa upande wa private sector kama kutakuwa na malimbikizo.

Mheshimiwa Spika, kwa nchi yetu hatuna utaratibu wa restrospectivity, tuna utaratibu wa pale sheria au agizo linapotolewa ama kanuni, itakapopitishwa ndipo kwenda mbele hatua hiyo inafanyika. Kwa hiyo, hili suala la mishahara litaanzia pale kima cha chini kitakapokuwa kimerasimishwa na kutangazwa na Serikali. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza taarifa iliyotolewa na Mheshimiwa Naibu Waziri nina mashaka nayo, kwa sababu wako wamachinga wengi Jiji la Arusha ambao wamekosa maeneo ya kufanyia baishara.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia taarifa ya Mheshimiwa Naibu Waziri ametuambia kwamba kwa sasa wao wamewatambua wamachinga 5,426 na kati ya hao wametoa vitambulisho kwa wamachinga 1187, je ni kwa nini wamachinga waliobaki mpaka sasa hivi hawajapata vitambulisho na wanaendelea kuchajiwa ushuru na Halmashauri ya Jiji la Arusha?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa mgambo ambao wanatumwa na Halmashauri ya Jiji la Arusha kupitia Mkurugenzi wa Jiji wamekuwa wanapora vitu vya watu vinakwenda kuwekwa kule depo vinaoza pia wanachukua fedha za watu nje ya utaratibu kiasi cha kuleta manyanyaso na kufanya hali ya kisiasa...

SPIKA: Mheshimiwa Gambo sasa hapo unachangia, Mheshimiwa Gambo ulishauliza maswali.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba taarifa hizi zimetoka ndani ya Halmashauri ya Jiji la Arusha kwa watendaji wa Serikali ambao wamejiridhisha idadi ya wamachinga walioko pale na idadi ya wamachinga ambao wamepewa vitambulisho. Pamoja na kwamba Serikali na Jiji la Arusha lilikuwa katika utaratibu wa kuwapanga wamachinga lakini utaratibuwa kutoa vitambulisho ulikuwa unaendelea sambamba na kuwapanga wamachinga; kwa hiyo nikutoe shaka katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, kuhusiana na kwa nini baadhi ya hawa wamachinga hawajapata vitambulisho; suala hili ni suala la kutoa elimu, kuhamasisha wale wamachinga wenye sifa waweze kutoa kwa hiari yao ili waweze kupata vitambulisho vile na kazi hii inaendelea kuelimisha ili hawa waliobaki nao wapate vitambulisho.

Mheshimiwa Spika, kuhusu mgambo kuvamia na kupokea fedha na kumwaga bidhaa za wananchi, Serikali ilishatoa tamko, kwamba katika shughuli za kuwapanga wamachinga nchini kote mgambo hawahusiki na hawatakiwa kuhusika kuleta bugudha yoyote kwa wafanyabiashara. Kwa hiyo nitoe maelekezo kwa Jiji la Arusha kusimamia maelekezo ya Serikali ili wafanyabiashara hawa wasibughudhiwe na mgambo sehemu yoyote. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, naomba kufahamu barabara ya kutoka uwanja mdogo wa Airport Arusha mpaka eneo la Kilombero kwa kiwango cha njia nne utaanza lini; na hasa ukizingatia kwamba barabara hii ikikamilika itasaidia kuondoa msongamano na changamoto ya mafuriko kwenye Kata za Ungalimitedi, Sombetini na Usunyai?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli barabara ya Airport kwenda Kilombero ni barabara ya muhimu kwenda njia nne; na ujenzi wa barabara hii kama ilivyo kwenye Majiji mengine utategemea sana upatikanaji wa fedha. Nadhani labda kwenye mpango huu tunaouendea, basi tutaomba tuweze kuanza kuweka mpango wa kuijenga barabara hii kwa kiwango cha barabara nne ili kupunguza msongamano katika Mji wa Arusha. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa mradi wa TACTIC pia upo kwenye Jimbo la Arusha Mjini na mnategemea kujenga stendi ya kisasa Bondeni City na lami maeneo ya Engosheraton na Olasiti na kwa kuwa mradi huu ulitegemea kuanza toka Julai, 2022. Je, ni nini changamoto inayochelewesha mradi huu kuanza kwa wakati maana miezi saba imeshapita mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulichelewa kidogo kwa sababu ya zile taratibu ambazo tulipaswa kuzifuata, lakini mpaka sasa tuko katika hatua nzuri. Kwa mfano, Jiji la Arusha lipo katika kundi la kwanza ambalo mwezi Februari, mwezi huu ambao tuko sasa, Serikali inatangaza kuwapata Wakandarasi watakaoanza kutekeleza na tunatarajia mchakato huu utakamilika mwezi Aprili na wakandarasi watakuwa site kujenga. Kwa hiyo, nimhakikishie Mbunge kwamba utekelezaji katika kundi la kwanza unaanza mwaka huu. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimwa Naibu Spika, na mimi napenda kuuliza swali la nyongeza; kwa maana ya kwamba tunafahamu changamoto ya walimu wa sayansi kwenye Jimbo la Arusha Mjini ni kubwa sana na hata kwa nchi nzima. Je, Serikali ina mpango gani wa kuja na mkakati Madhubuti wa kuondoa changamoto ya walimu wa sayansi wa nchi nzima?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba mpango wa Serikali namba moja ni kuajiri ajira mpya ambazo sehemu kubwa itakuwa ni kuchukua walimu wa sayansi. Mpango wa pili ni kuhakikisha kwamba sasa hivi sisi Ofisi ya Rais-TAMISEMI tukishirikiana na Wizara ya Elimu matarajio yetu ni kuanza kuwatumia hao walimu waliomaliza ambao watakuwa wanajitolea wenye professional hiyo kuhakikisha kwamba tunaondoa hiyo changamoto. Kwa hiyo tumejipanga vizuri kuhakikisha kwamba masomo ya sayansi tunapaa walimu na vifaa vilevile ili kuhakikisha wakati wote yanakuwa yanafundishwa, ahsante sana.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza majibu ya Serikali yamenishangaza kidogo, kwa sababu hapa wanazungumzia TanzaniteOne lakini ukiangalia TanzaniteOne tayari walishauza hisa kwa Sky Associate Group Limited.

Swali langu, kwa sababu hawa Sky Associate inaonekana kwamba walikuwa hawajasajiliwa na BRELA hapa Tanzania, je, mmiliki wa iliyokuwa TanzaniteOne ni TanzaniteOne wenyewe au hao Sky Associate Group Limited? Hilo ni swali langu la kwanza.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, wafanyakazi wa iliyokuwa TanzaniteOne hawajawahi kufukuzwa au kuondolewa kazini; je, hadi sasa wanazungumzia mahakamani miezi 11 lakini wanadai zaidi ya miezi 60 mpaka sasa.

Je, na hii miezi mingine iliyobaki watalipwa lini na kwa utaratibu gani na nini msimamo wa Serikali kwenye jambo hili? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Jimbo la Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa wamiliki wa mgodi kwamba kulikuwa na ubia ya mwingine zaidi ya TanzaniteOne pamoja na mwenzake aliyemtaja ni kwamba mgodi huu uliingiwa ubia kati ya TanzaniteOne na kampuni yetu ya Madini ya STAMICO. Kwa mujibu wa mikataba iliyokuwepo hakukua na mwingine na ndiye ambaye aliingia huu ubia na ndiye ambaye alikuwa mwendashaji wa mgodi na mwenye dhamana ya kuajiri na kufukuza wafanyakazi.

Mheshimiwa Spika, kwa swali la pili, malipo au madai wanaodai hawa wanaodai haki zao ambayo ipo kwenye kumbukumbu na ndio ambayo malalamiko haya yamefikia Wizarani ni hiyo shilingi bilioni 2.5 na sio bilioni 60 anayotamka na kama kuna madai ya nyongeza. Kwa kuwa suala hili tayari lipo bado kwenye mifumo ya kisheria, vyombo vyetu vya kisheria vitaendelea kulifuatilia na kufanyia kazi kwa mujibu wa taratibu na kanuni za Wizara husika.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa sababu changamoto ya barabara kwenye Jimbo la Malinyi inafanana na changamoto ya barabara kwenye Jimbo la Arusha Mjini. Naomba kuuliza swali kwa Mheshimiwa Naibu Waziri. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga barabara kutoka kwenye airport ya Kisongo mpaka eneo la Kilombero kwa sababu barabara hiyo inasababisha mafuriko sana kwenye Kata ya Unga Limited, Osinyai na Sombetini?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Barabara ya kutoka Kisongo kwenda Kilombero ni barabara ambayo ipo kwenye mpango na tayari usanifu unaendelea ili kukamilisha na kuweza kuijenga kwa kiwango cha lami na kuondoa changamoto kwa wakazi wa Arusha ambayo wanaipata sasa hivi. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa changamoto iliyopo Rungwe inafanana na Mradi wa Maji katika Jiji la Arusha.

Je, Wizara ina mpango gani kuhangaika na changamoto ya malalamiko ya wananchi ya bill kubwa za maji?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bill kubwa za maji tunaendelea kulifanyia kazi kwa kutoa ushirikiano wa wasoma mita na mtumia maji, lakini vilevile tuna mfumo ambao tayari baadhi ya mikoa umeanza kutumika kuona kwamba unatumiwa message una hakiki kwamba ndicho ulichokitumia kisha unaletewa bill sasa ya malipo. Hivyo bill kubwa ukomo wake umeshafikia kwa sababu ya unified billing system.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, kwanza sikubaliani na majibu ya Serikali kwenye swali langu la msingi kwa sababu ukizingatia kwamba sheria ni mwaka 2007, leo ni mwaka 2023 miaka 16 sasa bado Serikali inasema inatafuta fedha na huku wameweka vigingi kwenye maeneo ya wananchi lakini ingekuwa ni mwananchi ndiyo ameingilia kwenye hilo eneo Serikali ingeenda kumwondoa kwa nguvu. Baada ya maelezo hayo naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, ni lini sasa Serikali itawalipa fidia wananchi hawa? Swali la pili, kama Serikali haina uwezo wa kulipa fidia, kwa nini isiwaruhusu wananchi hawa wakaendeleza maendeleo hayo mpaka watakapokuwa tayari kuwalipa fidia?
NAIBU WAZIRI WA UCHUKUZI (MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye jibu langu la msingi kwamba Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kulipa wale wote ambao waliathirika na ujenzi huu wa Arusha Bypass kwa maana hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Wananchi wa Arusha waendelee kuwa na subira wakati Serikali inaendelea kutafuta fedha.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wananchi waruhusiwe kujenga maeneo haya. Nchi yetu inaongozwa kwa mujibu wa sheria na taratibu na sheria ya kuhifadhi barabara ambayo ilianza tangu mwaka 1932 enzi za ukoloni na ikarudiwa mwaka 1967 na tukatunga sheria mpya mwaka 2007 ambayo inataka hifadhi ya barabara kutoka kati kati ya barabara mpaka upande wa pili iwe mita 30 na kutoka kati kati tena upande mwingine iwe mita 30 kwa maana ya kwamba jumla ni mita 60.

Mheshimiwa Spika, kwa maana hiyo nimwombe Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote kwamba sheria hii lazima tuilinde na ikizingatiwa kwamba Arusha ni mjini tunahitaji pia kuendeleza miundombinu mizuri pale Arusha ili jiji hili la kitalii na kwa maana hiyo tuna hakika tukifanya vizuri katika suala la miundombinu hata watalii pia wataongezeka zaidi.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Naibu Waziri ametuambia kwamba wanatarajia kukamilisha mchakato wa zabuni mwezi Disemba, 2023.

Je, anaweza akatueleza leo kwamba ni lini wana mpango wa kutangaza tenda hii? Maana ili mchakato ukamilike lazima tenda iwe imetangazwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili la nyongeza; Mradi huu wa TACTIC mpaka sasa ulishatangaza tender kwa ajili ya kujenga barabara za lami za Engo Sheraton, Olasiti pamoja na Oljoro ambapo tunakwenda kujenga stendi. Tender ilitangazwa tarehe 27 mwezi Februari, na deadline ilikuwa ni tarehe 14 mwezi wa Nne. Leo miezi mitano imeshapita lakini mkandarasi bado hajakwenda site.

Je, ni lini watampeleka mkandarasi site ili barabara hizi za lami za Engo Sheraton, Olasiti na Oljoro zianze kujengwa mara moja?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Mashaka Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza lini tunatangaza tenda hiyo; kama nilivyosema tupo kwenye hatua za utaratibu wa manunuzi na siwezi kuwa certain sana kusema lini exactily lakini nakuhakikishia tu kwamba by Disemba mwaka huu tutakuwa tumekamilisha taratibu zote za manunuzi, na mkandarasi kwenda site kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa mradi huu.

Mheshimiwa Spika, pili kuhusiana na hii tenda ya ujenzi wa barabara hizi ambazo mpaka sasa zaidi ya miezi minne, mitano mkandarasi hajaenda site. Naomba nitumie fursa hii kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, TAMISEMI, kutoa maelekezo kwa Meneja wa TARURA Mkoa wa Arusha, lakini pia Halmashauri ya Wilaya ya Arusha, kwa maana ya Jiji la Arusha, kuhakikisha wanamfuatilia mzabuni huyo kwa maana ya mkandarasi huyo aanze kazi mara moja kwa kufuata taratibu. Kama kuna mkwamo wowote Ofisi ya Rais- TAMISEMI tutaingilia kati kuhakikisha tunakwamua na kazi inaendelea, ahsante.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri unaonaje hilo agizo lako lingeenda kwa mameneja wote ambao mradi huo wa TACTIC unaenda?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Spika, napokea na naomba niseme kuwa kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri naelekeza kwa Mameneja wote wa TARURA katika mikoa na wilaya ambazo zinatekeleza Mradi wa TACTIC kuhakikisha kuwa wanasimamia kwa karibu hatua zote za manunuzi, lakini pia kuhakikisha kuwa wakandarasi wanafika site kwa ajili ya kuanza utekelezaji wa miradi hiyo mara moja. Ahsante.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa Jiji la Arusha limetenga eneo la ekari tano kwenye Kata ya Terrat kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama mpya ya mwanzo; je ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mahakama hii ya mwanzo kwenye Kata ya Terrat?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mrisho Gambo, Mbunge wa Arusha Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha ambao tunashukuru Bunge lako tukufu lilitupitishia bajeti ya zaidi ya bilioni 57 fedha za nje pamoja na bilioni 31 fedha za ndani, tumepanga kujenga mahakama zaidi ya 60 na miongoni mwa maeneo ambayo tutakwenda kujenga ni eneo hili la Terrat pale Arusha. Kwa hiyo, Mheshimiwa Gambo kuwa na amani mwaka huu tunajenga Mahakama katika eneo la Terrat.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na kwa kuwa madini ya Tanzanite yanaruhusiwa kuuzwa duniani kote ikiwa ni pamoja na India na Marekani.

Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa vibali ili madini hayo pia yaweze kuuzwa kwenye mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Mwanza na nchi ya Zanzibar?
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini napenda kumjibu Mheshimiwa Gambo kwamba madini ya Tanzanite ni madini ya kipekee kabisa ambayo yanapatikana nchini Tanzania tu na kwa ajili hiyo Serikali iliweka utaratibu wa kusimamia uzalishaji, uchakataji, uongezaji wake thamani palepale Mererani. Lakini katika kipindi tulichoko sasa hivi tuko katika hatua za kufanya tathmini ya utaratibu uliowekwa na Serikali ambapo baada ya kujiridhisha kwamba kuna utaratibu mwingine mzuri wa kuruhusu madini hayo yauzwe kila mahali ndani ya nchi na nje ya nchi, bila kuathiri uhalisia wa hali iliyokuwepo ya mwanzo ya utoroshaji wa kiholela tutakwenda kuweka utaratibu mahususi ili madini hayo yaweze kuanza kuuzwa popote pale maadam pia yatakuwa yameshaongezewa thamani na kupewa vibali vya kutoka ndani ya eneo la Mererani ambalo ni eneo tengefu kwa sasa.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia majibu ya Serikali, yanaonesha kwamba zoezi hili lilianza mwaka 2019 na mpaka leo ni takribani miaka mitano, wameweza kufungia wananchi 345 ambayo ni sawa na asilimia 0.285 kwa miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizingatia kwamba wananchi wa Jimbo la Arusha Mjini wamekuwa wanalalamika kwa muda mrefu sana kuhusiana na bili kubwa za maji na kubambikiwa bili; je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na changamoto hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ni kwamba, kama kwa miaka mitano tumeweza kufungia wananchi kwa maana ya 345 kati ya wananchi 120,899 ambao wanatakiwa kufungiwa mita za LUKU za namna hiyo; je, Serikali imejipangaje kuweka timeframe kuhakikisha kwamba wananchi wote 120,899 wanafungiwa mita za maji kama za LUKU?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujipanga kuhusiana na ubambikaji wa bili kwa wananchi, hili tayari tumeshalifanyia kazi kubwa sana. Zoezi hili limeanza taratibu kwa sababu ya kutoa elimu na kuhakiki hizi dira ambazo tumekuwa tukizitoa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba tumejipangaje sisi kama Wizara, tayari tumetoa fursa kwa vyuo vyetu vya ufundi hapa nchini; Chuo cha Ufundi Arusha, pamoja na Chuo cha Ufundi cha Dar es Salaam, (Dar es Salaam Institute of Technology) ambao sasa tayari wanaendelea kutengeneza mita hizi. Lengo ni kuona tunataka kusambaza mita kwa bei nafuu. Kwa sababu mita za awali tulikuwa tumezitoa nje, bei kidogo ilikuwa juu kwa wananchi, nasi kama Serikali tunaangalia uwezekano wa kumpunguzia gharama za maisha mlaji wa mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la ufungaji mita za malipo kabla, zitaendelea vizuri na siyo tu kwa Arusha, bali nchi nzima. (Makofi)
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia majibu ya Serikali, yanaonesha kwamba zoezi hili lilianza mwaka 2019 na mpaka leo ni takribani miaka mitano, wameweza kufungia wananchi 345 ambayo ni sawa na asilimia 0.285 kwa miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukizingatia kwamba wananchi wa Jimbo la Arusha Mjini wamekuwa wanalalamika kwa muda mrefu sana kuhusiana na bili kubwa za maji na kubambikiwa bili; je, nini kauli ya Serikali kuhusiana na changamoto hii? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili ni kwamba, kama kwa miaka mitano tumeweza kufungia wananchi kwa maana ya 345 kati ya wananchi 120,899 ambao wanatakiwa kufungiwa mita za LUKU za namna hiyo; je, Serikali imejipangaje kuweka timeframe kuhakikisha kwamba wananchi wote 120,899 wanafungiwa mita za maji kama za LUKU?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mrisho Gambo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujipanga kuhusiana na ubambikaji wa bili kwa wananchi, hili tayari tumeshalifanyia kazi kubwa sana. Zoezi hili limeanza taratibu kwa sababu ya kutoa elimu na kuhakiki hizi dira ambazo tumekuwa tukizitoa nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwamba tumejipangaje sisi kama Wizara, tayari tumetoa fursa kwa vyuo vyetu vya ufundi hapa nchini; Chuo cha Ufundi Arusha, pamoja na Chuo cha Ufundi cha Dar es Salaam, (Dar es Salaam Institute of Technology) ambao sasa tayari wanaendelea kutengeneza mita hizi. Lengo ni kuona tunataka kusambaza mita kwa bei nafuu. Kwa sababu mita za awali tulikuwa tumezitoa nje, bei kidogo ilikuwa juu kwa wananchi, nasi kama Serikali tunaangalia uwezekano wa kumpunguzia gharama za maisha mlaji wa mwisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, nimtoe hofu Mheshimiwa Mbunge kwamba zoezi la ufungaji mita za malipo kabla, zitaendelea vizuri na siyo tu kwa Arusha, bali nchi nzima. (Makofi)