Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Geoffrey Idelphonce Mwambe (1 total)

MHE. DOROTHY G. KILAVE Aliuliza:-

Serikali ilitenga eneo la Kurasini EPZ tangu mwaka 2014 kwa ajili ya uwekezaji lakini hadi sasa eneo hilo halijaendelezwa kama ilivyokusudiwa.

Je, kwa nini Serikali isirejeshe eneo hilo kwa Halmashauri ya Temeke ili lipangiwe shughuli za maendeleo?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO K.n.y. WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Temeke kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda na Biashara Serikali kupitia Mamlaka ya EPZ ilianza mchakato wa kutwaa ardhi eneo la Kurasini mwaka 2014 kwa madhumuni ya kujenga Kituo cha Biashara na Ugavi wa Vifaa. Hatua mbalimbali za kuendeleza eneo hilo zimefanyika zikiwemo ulipaji wa fidia, kusafisha eneo kwa kubomoa majengo yaliyokuwepo, kufanyika kwa upembuzi yakinifu wa awali na kupatikana kwa hatimiliki. Hatua inayoendelea sasa ni tathmini ya mazingira na maandalizi ya mpango kabambe (conceptual master plan) inayofanywa kwa kushirikiana na Bodi ya Kahawa.

MheshimiwaNaibu Spika, Wizara katika Bajeti yake ya mwaka 2020/2021 imetenga fedha kwa ajili ya uendelezaji wa miundombinu ya mradi awamu ya kwanza ikiwemo ujenzi wa uzio kuzunguka eneo la mradi. Tayari Mamlaka ya EPZ imeingia mkataba na Kitengo cha Ujenzi cha Jeshi la Kujenga Taifa kwa ajili ya ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa nia ya Serikali katika kutekeleza mradi huu wa kielelezo kwa mujibu wa Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa iko pale pale na pia nitumie fursa hii kuomba ushirikiano wake na Halmashauri ya Wilaya ya Temeke kwa ujumla ili kufikia azma ya Serikali kupitia uendelezaji wa mradi huu kwa malengo yaliyokusudiwa. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Dorothy Kilave swali la nyongeza.

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Waziri, lakini naomba sasa niseme kwamba sasa ni miaka karibu saba tangu mmelitwaa hili eneo.

Je, haiwezekani kwamba mtachukua tena miaka saba kwa ajili ya kulirekebisha na kuweka mpango huo? Niombe basi kama nilivyosema kwamba wananchi wa Temeke tunatamani kujenga shule za sekondari na msingi kwa sababu tunazaliana sana na maeneo mijini sasa hivi hakuna. Niseme tu kwamba tuombe sasa Wizara yako itupe eneo hili ili sisi katika miaka hii ambayo tumeambiwa tujenge shule za sekondari pamoja na msingi basi tuyapate kwa sababu naona mtakwenda tena miaka saba ijayo katika kutengeneza hili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili; je, Serikali yetu sasa ina mpango gani wa kumalizia fidia kwa wananchi wa maeneo ya jirani karibu na pale ambapo mmetwaa lile eneo lakini yapo maeneo Shimo la Udongo ambapo mlitakiwa kuyatwaa lakini bado hamjalipa fidia. Naomba maswali yangu haya mawili tuweze kujibiwa. (Makofi)