Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Geoffrey Idelphonce Mwambe (9 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
WAZIRI WA VIWANDA NA BIASHARA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kunifanikisha kuwa hapa leo. Pili nimshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa imani yake kubwa aliyokuwa nayo kwangu kunipa utumishi wa kusimamia jukumu la Wizara yetu ya Viwanda na Biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nisisahau chama changu, Chama cha Mapinduzi kwa imani kubwa waliyokuwa nayo wajumbe wetu wa Mkutano Mkuu wa Jimbo la Masasi Mjini. Pia niwashukuru wananchi wa Masasi kwa kunipa kura nyingi na kunipa jukumu la kuwawakilisha kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile napenda kuishukuru sana familia yangu akiwemo mke wangu Tumaini Jasson Kyando na watoto wangu King King, Caren, Catherine kwa imani kubwa waliyokuwa nayo na kunivumilia kwa kipindi kirefu cha utumishi wangu ambapo muda mwingi nakuwa nje ya nyumbani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza kabisa tumshukuru sana Mheshimiwa Rais. Kimamlaka presidential speech is a policy speech. Rais anapata absolute powers kutoka kwenye Katiba, ana mamlaka yote. Mamlaka ya mwananchi mmoja mmoja yote yamekusanywa kupitia kura wakampa yeye. Kwa hiyo, tamko lake ni tamko la wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sisi watumishi ambao tunatumikia kwa nafasi zetu za kuongoza Wizara kwa niaba yenu, ni maelekezo na ni maagizo. Kwa hiyo, mwanzo kabisa napenda kusema kwamba naunga mkono hoja na sisi tumejipanga kutekeleza. Kazi yetu kubwa ni kutekeleza na tumeshaanza kuifanyia kazi hotuba hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, bahati nzuri sana napenda nikumbushe kwamba hotuba ya Mheshimiwa Rais zote mbili ikiwemo hii ya terehe 13 Novemba 2020, zinawiana na Ilani ya Uchaguzi ya CCM ya 2020 - 2025. Yote ambayo ameyaongea ni yale ambayo yako kwenye kurasa 303 ya Ilani ya CCM ambayo wengi wetu hapa tulikuwa tunainadi na bahati nzuri pia kila mmoja humu ndani hakuna ambaye amesema kwamba hotuba ile kuna maeneo hakubaliani nayo isipokuwa msisitizo ni namna sisi kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mlituambia wiki ijayo tutakuwa na mjadala wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitatu ukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Rais inajikita huko pia. Baada ya Mpango wa Kwanza wa Maendeleo ambao tulikuwa tunajikita kwenye kutengeneza miundombinu ikiwa ni kama capillaries za uchumi, wa pili tukasema tujenge viwanda lakini Mpango wa Tatu tunachukua sasa mafanikio ya kipindi cha kwanza na cha pili tunaunganisha kwenye mpango huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukipitia hotuba ile ukurasa wa 10 – 26 kuna maeneo mengi ambayo Mheshimiwa Rais ameyaelekeza ambayo yanagusa kwa namna moja au nyingine maeneo ya viwanda na biashara. Hivyo napenda kupitia hotuba hiyo kuangalia michango mbalimbali ya Waheshimiwa Wabunge ili tuweze kujua namna ambavyo sisi kama Wizara ya Viwanda na Bishara tumejiandaa. La kwanza, ni utekelezaji wa blue print. Kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge walionesha kama vile tunahitaji tuanze kutekeleza lakini naomba niwahakikishie kwamba blue print tumeanza kuitekeleza tangu mwaka juzi na baadhi yenu mnafahamu hata ile iliyokuwa TFDA, sasa hivi inaitwa TMDA kutokana na utekelezaji wa blue print. Kwa hiyo, tutaenda kuhakikisha kwamba ile comprehensive action plan ya blue print tunaitekeleza ipasavyo na kuja na mbinu mpya zaidi ya kuweza kutekeleza vizuri zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwa upande wa masoko imezungumzwa sana hapa kwamba bidhaa nyingi zinakosa masoko. Naomba niwahakikishie tunaenda kuiboresha taasisi/ mamlaka yetu ya Maendeleo ya Biashara (TANTRADE) ambayo kimsingi imebeba jukumu la Board of Internal Trade (BIT) and Board of External Trade (BET). Bodi hizo mbili ziliunganishwa zikatengeneza TANTRADE, lengo lake kubwa au majukumu yake makubwa ni kutafuta masoko ya mazao yetu na bidhaa zetu kwa masoko ya ndani kuunganisha kutoka mkoa mmoja na mwingine, masoko ya kanda na masoko ya Kimataifa kupitia multilateral trading system ambayo sisi ni Wajumbe. Kwa hiyo, naomba niwahakikishie tu Waheshimiwa Wabunge kwenye hili tutaenda kupambana kuhakikisha masoko ya bidhaa zetu yanapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna maboresho ya taasisi zetu. Chuo cha Elimu ya Biashara (CBE) kiko chini ya Wizara ya Viwanda na Biashara, nimewaambia kwamba tuangalie course content. Tusingependa na kwa kipindi hiki sio vyema kutengeneza business administrators yaani tunatengeneza wasimamizi wa biashara, biashara ya nani? Mimi nimewaambia wakae, waje na mpango mpya tutengeneze course content ambazo zinamjenga asilimia 70 yule mtoto yeye ndiyo akawe mfanyabiashara halafu asilimia 30 iwe ndiyo kusimamia biashara. Unakuwa business administrators wengi wanasimamia biashara ya nani? Kwa hiyo, tunaenda kuiboresha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kama WIzara ya Viwanda na Biashara, tutakuja na Programu ya Miliki Kiwanda ambayo nitaomba sana Waheshimiwa Wabunge kwa sababu Mheshimiwa Rais kwenye hotuba yake ametamani nyie muwe sehemu ya mabilionea mshiriki. Tutakuja na Programu ya Miliki Kiwanda ili kokote ulikokuwa kwenye Jimbo lako, wilaya yako tutengeneze utaratibu wa kuanzisha kiwanda wewe Mbunge ukiwa ni champion kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna masuala ya sekta binafsi. Sekta binafsi yetu ni changa sana tunahitaji kuijenga kwenye maeneo mawili. La kwanza, kuwapa fursa ya kuweza kufanya biashara. Hii tumezungumza mara kwa mara na nashukuru pia Mheshimiwa Waziri Mpango mara baada ya kuapishwa tu alikutana na uongozi wa Mamlaka ya Mapato Tanzania aliwasisitizia, kufunga biashara au kiwanda cha mtu iwe ni baada ya Commissioner General kutoa kibali. Biashara zote ziko chini ya leseni za viwanda na biashara, napenda kusisitiza sana, tuilee sekta binafsi lakini pia tuwaelimishe kwa upande wa integrity, lazima na wao wawajibike upande wao kuwa na integrity kwa Serikali ili iweze kuwaamini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia siku hii ya leo. Kikubwa zaidi ningependa sana kuwashukuru viongozi wetu wa kitaifa, Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, lakini pia na Makamu wa Rais Dkt. Philip Isdor Mpango na Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, lakini pia na Baraza la Mawaziri lote kwa kuendeleza majukumu ambayo tumekuwa nayo katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nisingependa kutoka hivi hivi bila kuzungumza tatizo ambalo limetupata kitaifa, kutoa pole kwako lakini pia na familia ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, lakini pia na Watanzania wote kwa ujumla kwa kuondokewa na kipenzi chetu, jemedari, kiongozi mwenye maono na hatimaye kumfikisha kwenye nyumba yake ya milele kule Chato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ningependa sana kutoa shukrani zangu kwa kamati mbili za Utawala na Serikali za Mitaa, kwa maoni yao ambayo yalikuwa ni mapana, very extensive. Tunashukuru sana na yale maoni tumeyachukua yote na tuwahakikishe kwamba tunakwenda kuyafanyia kazi, kuhusiana na namna ambavyo tutakuza uwekezaji kwenye nchi yetu. Pia Kamati ya Katiba na Sheria ambayo pia imetoa maoni mengi, lakini kipekee Bunge lako Tukufu, Waheshimiwa Wabunge wameweza kutoa maoni mengi, kwa sababu tunafahamu suala la uwekezaji ni suala pana suala kubwa na ndio linajenga uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, kimsingi hoja kubwa ilikuwa ni kujenga mazingira wezeshi kwa ajili ya uwekezaji. Pia kuwa na mtazamo chanya kuhusu masuala ya uwekezaji kwenye nchi yetu na kwa kutambua kwamba kila taasisi isijiangalie peke yake, lazima itambue kwamba tuna sababu nyingi za kuvutia uwekezaji kwenye nchi yetu. Eneo la kwanza ni ajira kwa vijana wetu, tunafahamu kwamba Ilani ya CCM ya Uchaguzi lakini pia kwenye Mpango wetu wa Maendeleo tumepanga kutengeneza fursa za ajira zaidi ya milioni nane.

Mheshimiwa Spika, pia tunataka ukuaji wa uchumi wetu ambao ni mkusanyiko wa shughuli mbalimbali za kiuchumi ambazo zinafanywa na sekta binafsi lakini na Serikali Kuu na Serikali za Mitaa ziweze kufikia angalau asilimia nane kwa kila mwaka. Tafsiri yake ni kwamba uzalishaji wote wa mwaka huu ukitoa uzalishaji wa mwaka jana ukigawanya kwa uzalishaji wa mwaka jana ukizidisha mara 100 basi ikupe asilimia nane ndio tafsiri yake, lakini pia tunafahamu kwamba tumeingia kwenye uchumi wa kati kabla muda wetu ambao tuliupanga mwaka 2025 na hili ni moja ya mafanikio makubwa sana ambayo sijui kwa nini hayazungumzwi kwa uzito.

Mheshimiwa Spika, tumeweza kufanikiwa kuingia kwenye uchumi wa kati mapema zaidi kwa sababu ya juhudi kubwa tulizoziweka kwenye maeneo mbalimbali ya uzalishaji ikiwemo kuvutia uwekezaji. Tafsiri yake labda tuweze kuiweka vizuri tu, kuna kitu tunaita GNI ambayo ni GDP unaiweka kwenye market prices ambayo unapata gross national income, ukigawanya kwa idadi ya watu ndio unapata per capital income ambayo sasa ile ndio imetufikisha pale kwenye 1,080 ambayo ni kiwango cha mwanzo cha kuingilia ngazi ya uchumi wa kati.

Kwa hiyo hata baadhi ya michango tulikuwa tunaisikia hapa tumeingia kwenye uchumi wa kati lakini kule vijijini hatuoni, tafsiri yake sio hiyo.

Mheshimiwa Spika, kule vijijini kimsingi tunaona kwamba badala mtu kutembea kilometa tano kufuata zahanati, basi anatembea kilometa moja au mita 500 kwa sababu zahanati imejengwa kwenye kituo chake cha makazi. Pia huduma nyinginezo za usafiri ambazo zamani ulikuwa uamke saa 10 uweze kupata gari, lakini sasa hivi gari unasimama tu popote unaweza kupata. Vile vile miundombinu yetu imeboreshwa sana. Sasa hivi kila familia ina angalau pikipiki na gari, vitu ambavyo zamani tulikuwa tunasema ni luxury sasa hivi tumevichukua kama ni necessity na ndio maana mahitaji ya maendeleo yetu yanakuwa yanaongezeka kila siku.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa kweli tumepiga hatua kubwa. Haya yote yametokana na uamuzi wa Serikali kuweza kufungua fursa za uwekezaji kwenye nchi yetu, kuruhusu private sector lakini pia kuruhusu Serikali yenyewe kuweza kuwekeza.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba nijielekeze kwenye maeneo ya uwekezaji hususan yake ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge hapa.

Mheshimiwa Spika, la kwanza naomba niwatoe hofu Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu, kwamba mikakati na mipango ambayo iliwekwa na Serikali ya Awamu ya Tano chini ya hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli akiwa na msaidizi wake wakati huo, Makamu wa Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan walifanya wote, nalichukulia ni kama vile uendeshaji wa ndege, ndege zina Pilot na co-pilot, tuna bahati kwamba sasa hivi aliyekuwa co-pilot wakati ule ambaye alishiriki kwenye program za manifesto kuangalia manifesto ya ndege, kutengeneza mission plan ya kwamba turuke twende destination gani, tupitie route ipi, hali ya hewa ikoje, walipanga wote wawili, ndio maana kuna mwendelezo na pia tumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kusema kwamba kazi iendee sio ianze upya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wale wote wanaojaribu kuutoa ushauri wa hapa na pale kuhusiana na nini akifanye, natamani sana wampe nafasi, afanye kazi yake kwa sababu anaifahamu, alikuwepo kwenye kupanga mipango na yeye ni sehemu ya mipango hii ambayo tunaitekeleza kwa sasa. Ushauri mwingi ambao unatolewa, ningependa sana kuwashukuru lakini tumuache Mheshimiwa Rais, anafahamu wapi ataifikisha nchi yetu kwa sababu tunayo Dira ya Maendeleo ya Taifa, tunayo Ilani ya CCM, tunao Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano awamu ya tatu, ile awamu ya pili yeye mwenyewe alishikiri, lakini hii Ilani ya CCM yeye alishiriki kuipitisha kama Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, lakini pia kama msimamizi wa shughuli za Serikali pia akiwa kama ni Makamu wa Rais, kwa hiyo anafahamu wapi anataka kuipeleka nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie mageuzi makubwa ambayo yamefanywa kwenye nchi yetu kwa upande wa uwekezaji ikiwa ni pamoja na kuunda Wizara ya Uwekezaji, walifanya wote hayati Dkt. John Pombe Magufuli akiwa na Mama Samia Suluhu Hassan kama Makamu wake. Pia na kitendo cha yeye si tu kuamua kuibakiza Wizara ya Uwekezaji, lakini kuipa hata Katibu Mkuu na iwe Wizara Kamili, ni uthibitisho tosha kwamba amedhamiria kukuza mazingira ya uwekezaji nchini, lakini pia kuhakikisha kwamba tunakuza shughuli mbalimbali za uwekezaji kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, la pili, kuna mapitio ya Sera ya Taifa ya Uwekezaji, Sera yetu hii ni ya siku nyingi, ni ya mwaka 1996, kwa hiyo kwa kiasi kikubwa ni kama inahitaji maboresho, inahitaji kuhuishwa ili mambo mapya na changamoto ambazo tumezipata kwenye utekelezaji wa sera ile ya zamani tuweze kuyaingiza kwenye sera mpya na ituongoze vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia kuna sheria yenyewe ya uwekezaji, baada ya kupitisha Sera ya Uwekezaji mwaka 1996, mwaka 1997 Bunge lako Tukufu likapitisha Sheria Na. 38 ili iweze kutuongoza sasa katika utekelezaji wa ile sera kwa upande wa sheria. Hiyo tunafanya mapitio na tumefikia hatua ya juu sana.

Mheshimiwa Spika, nafikiri muda siyo mrefu Bunge lako Tukufu litapata nafasi ya kuipitia hiyo sheria ya uwekezaji na ikiwezekana tupate hiyo sheria mpya ya uwekezaji ambayo itabeba mambo mengi ambayo Waheshimiwa Wabunge wamependekeza. Kwasababu wakati mwingine tulikuwa tunakwazwa na sheria yenyewe huwezi kufanya zaidi ya pale.

Mheshimiwa Spika, pia kuna eneo la maboresho kutokana na taarifa ambazo zinatolewa na International Finance Cooperation (IFC) ambayo ni sehemu ya World Bank Group hii Benki ya Dunia ambayo inatupima sisi Tanzania na nchi zingine 192 duniani namna gani mazingira yetu ni wezeshi kwa upande ufanyaji wa biashara ile easy of doing business ambako tumekuwa rent kwenye numbers ambazo siyo nzuri sana ambazo sisi tungetamani tubadilike kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tangu mwaka 2010 baada ya sisi kuingizwa kwenye huo mpango Serikali imekuwa ikifanya mapitio kupitia mpango wa maboresho ili kuhakikisha kwamba maeneo ambayo yanaainishwa ambayo ni maeneo 11 kuanzia unaposajili kampuni BRELA mpaka unapofunga kampuni BRELA, na hapa katikati kuna vigezo vingi namna ya kupata umeme kupata mikopo na ulipaji wa kodi na mazingira kama hayo kwa hiyo, vigezo vyote vinaangaliwa lakini pia na blue print.

Mheshimiwa Spika, mtakumbuka mwezi Mei 2019 Baraza la Mawaziri lilipitisha blue print ni maarufu kama blue print lakini ni mpango wa maboresho ya mazingira ya ufanyaji biashara kwenye nchi yetu na hii ni mpango wetu sisi is a home grown program ni ya kwetu sisi hakuna Benki ya Dunia, hakuna IMF waliyotuletea ni dhamira ya Serikali ya Awamu ya Tano ambayo Mama Samia Suluhu Hassan kama Makamu wa Rais wa wakati huo naye alikuwa ni sehemu ya huo mpango walipitisha na kuhakikisha kwamba tunaitekeleza ipasavyo na nikuhakikishie sana na Bunge lako Tukufu kwamba tunaenda kuisimamia hilo na tuhakikishe kwamba tunaitekeleza ipasavyo na kujenga mazingira wezeshi kwa upande wa biashara.

Mheshimiwa Spika, lakini pia mabadiliko ya sera na sheria mbalimbali za kifedha na kikodi Bunge lako tukufu limekuwa likipitisha hapa finance act kuangalia maeneo yale ambayo yametajwa kodi tozo mbalimbali ambazo zinachajiwa na taasisi na halmashauri zetu za wilaya au Serikali za Mitaa ili tuhakikishe kwamba tunajenga mazingira wezeshi kwa upande wa maeneo ya biashara na uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, pia yako maboresho ya utendaji wa kituo chetu cha uwekezaji kuna mambo mengi ambayo yamefanyika ingawa majukumu yake ya kisheria yanatakiwa yatimizwe kulingana na sheria inavyotaka. Pale kwenye kituo cha uwekezaji tumetengeneza well stop facilitation center ambako watumishi wa taasisi mbalimbali sasa hivi wako taasisi 14 pale kuna watumishi kama 25 ambao wanakaa pale kuna watumishi wa TRA, kuna watumishi wa BRELA, watumishi wa Uhamiaji, kuna watumishi wa Idara ya Kazi. Lakini pia watumishi wa NEMC, watumishi wa OSHA wa NIDA wako pale wanatimiza majukumu ya taasisi zao katika kufanikisha uwekezaji lakini wakitokea ndani ya kituo cha uwekezaji na hii yote ilikuwa ni katika kujenga mazingira wezeshi na kutoa usumbufu kwa upande wa uwekezaji kuzunguka kwenye hizo na kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, changamoto kubwa iliyokuwepo ni kwamba kuimarisha na kuhakikisha kwamba tunakuwa na watumishi ambao wanamaamuzi pale ndani ya taasisi hilo tunaenda kulifanya na tunataka hii sheria yetu ikipita mpya tuhakikishe kwamba wanaokaa pale ni watu wenye maamuzi siyo tena watumishi ambao wanatakiwa kila mara kupiga simu kwenye taasisi zao kuandika email au kupeleka mafaili kwa hiyo itachelewesha kwenye biashara zetu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna mfumo tuliuweka wa National Investment Facilitation Committee ambao wakuu wa taasisi zote ambazo kwa namna moja au nyingine huduma zao zinagusa wawekezaji wanakutana chini ya uwenyekiti wa Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Uwekezaji na kupitia changamoto mbalimbali na naomba nikuhakikishie kupitia Forum hii changamoto 53 zilitatuliwa na mojawapo ilikuwa ni kiwango cha utozaji wa ada wa NEMC pale ambapo mtu anataka au mwekezaji anataka kupata cheti cha NEMC anatakiwa alipie zamani ilikuwa ni asilimia ya mtaji lakini baadaye kupitia kikao hiki tukaja kubaini hapana huwezi kufanya asilimia ya mtaji tafsiri yake mtu kama anawekeza bilioni 100 basi ana 0.03 ya bilioni 100 ni hela nyingi sana kwa hiyo kupitishie EIA ripoti yake apate certificate.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukakubaliana kwamba watengeneze regulation upya na bahati nzuri Mheshimiwa Waziri wa wakati huo akaisaini wakatengeneza band ya maeneo kama 14 ambayo yanasema tu kwamba kuanzia mtaji 0 mpaka labda milioni 5 basi utalipia shilingi 50,000 tu. Kwa hiyo, katika milioni 5 mpaka labda milioni 20 utalipia labda 100,000 tu. Tulipata mafanikio sana kupitia huu mfumo na tutaendelea kuboresha ikiwemo mfumo unaotumika kwaajili ya vibali vya kazi ni mfumo ambao umetengenezwa pale TIC kwaajili ya kufanikisha hii na ni imani yetu kwamba tutaendelea kutengeneza mifumo mingi zaidi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ilikuwa ni uanzishaji na uendelezaji wa land bank au akiba ya ardhi ya uwekezaji. Uwekezaji wote unafanywa kwenye ardhi changamoto kubwa imekuwa ni kupata ardhi kwa wakati. Lakini pia na mchakato wa uhulishaji wa ardhi.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna maeneo mawili moja watu binafsi na Serikali kuhakikisha kwamba ikiwemo Tawala za Mikoa na Halmashauri zetu kupima maeneo ya ardhi na kuhakikisha kwamba ile ardhi tunaileta kwenye kituo cha uwekezaji ili tuweze kuinadi kwa wawekezaji uweze kupata urahisi wa kuipata urahisi wa kuipata ile lakini gharama zote za ulipaji na nini atalipa huyo mwekezaji kikubwa Zaidi ni kwamba asipate muda mrefu wa kuipata hiyo ardhi.

Mheshimiwa Spika, lakini kingine tuna National Land Allocation Committee ambayo inaratibiwa na Wizara ya Ardhi ambayo imekuwa ikigawa hii ardhi kulingana na mahitaji kwa wawekezaji.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kuhusu kuondoa urasimu na kufanikisha uwekezaji. Hili Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amezungumza kwa kauli nzito angetamani na angependa tuondoe urasimu kwenye maeneo yetu tutambue wajibu wetu kama watendaji kama watumishi na sisi kama Wizara ya Uwekezaji lakini pia Ofisi ya Waziri Mkuu, tutaenda kufanya, bahati nzuri Mheshimiwa Waziri Mkuu ndiyo msimamizi wa shughuli za Serikali tutaendelea kusisitiza hili tuwajibike kwa kujua kwamba tutaisaidia nchi yetu kwenye kufikia kwenye malengo yale yaliyoainishwa kwenye dira ya maendeleo ya miaka 25 lakini pia na mipango yetu ya maendeleo ya miaka mitano mitano ambayo sasa hivi tuko kwenye mwaka wa tatu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kutambua kwamba tuna ajira kwa vijana lazima tutengeneze ajira kwa vijana lakini pia kuna kutengeneza soko la haraka la wakulima wetu. Kwahiyo tukifanikisha uwekezaji maana yake tunasababisha wakulima hawa wapate soko la haraka kwasababu kutakuwa na wanunuzi hapa ndani. Lakini pia tunahitaji fedha za kigeni ili uchumi wetu uwe imara.

Mheshimiwa Spika, reserve ya fedha za kigeni ni muhimu sana ili iweze kushikilia thamani ya shilingi la sivyo tutakuwa tukihitaji kulipia huko nje kama ni madeni ama au ni uagizaji wa vitu ni lazima tutoe fedha nyingi za Kitanzania tupate dola moja na kufanya sasa ile exchange rate kwenda juu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuwa na pesa ambayo iko tayari kuweza kulipia hizo external obligations kwa hiyo kuna haja sana ya kuvutia uwekezaji tupate fedha za kigeni lakini pia tuweze ku-export hivi vitu vyetu lakini pia kuna masoko ya kikanda na kimataifa ambayo tumesainiwa iko EAC, SADC and International, AGOA ambayo tumesaini kwa hiyo, naomba sana niwahakikishie Bunge lako tukufu kwamba tunaenda kuweka juhudi kubwa sisi kama…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, napenda sana kukushukuru napenda kuunga hoja mkono ahsante sana (Makofi).
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, napenda kushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia na mimi hoja tatu ambazo zimewekwa mbele yetu lakini kipekee nitajikita kwenye hoja zilizoletwa na Kamati ya PAC.

Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kumshukuru sana Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, kwa juhudi kubwa anazozifanya za kuhakikisha kwamba tunatoa huduma bora kwa wananchi wetu na kuzingatia value for money kwenye miradi yetu, lakini tunaongeza makusanyo na kuboresha hali ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, naichukulia hali ya ukaguzi uliofanywa kwenye taasisi lakini pia na Wizara kama huduma ambayo CAG anaitoa kwa Bunge. Na ninachukulia kwamba sisi Wabunge ni Madaktari na tumemuomba CAG atuangalizie mgonwa ambae ni Serikali na CAG yeye ni mtaalam wa Maabra. Baada ya ukaguzi wa damu, CT scan mRI akatuletea matokeo na matokeo ambayo ametuletea Kamati inawasilisha kwenye Bunge kama jopo la Madaktari ili tuweze kujadili na kutoka na maazimio ya ni namna gani mgonjwa wetu atatibiwa.

Mheshimiwa Spika, tumesikia hoja za wajumbe mbalimbali lakini pia za Mwenyekiti wetu wa PAC kuhusiana na yale tuliyoyabaini kwenye majadiliano yetu na CAG pia na taasisi husika. Kuna changamoto nyingi tumeziona lakini ninaweza kuzipanga katika maeneo matatu au manne.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ni mikataba. mikataba mingi ambayo inaonekana imesainiwa inatugharimu mabilioni ya pesa kama Taifa. Ukiangalia kwa mfano bilioni 355 ambazo tunaenda kuzilipa kwa Symbion, ukigawa milioni tano tano kwa wanafunzi wetu wa vyuo vikuu, tungeweza kuwahudumia wanafunzi 71,715 kwa kuwapa mikopo; lakini hiyo tunakwenda kuwalipa Symbion tu kwa mkataba wa awali ambao kimsingi ulisainiwa under emengency power plan, mwaka 2006/2007. Vile vile bado ukaongezwa mwaka 2008 ukasogwezwa ukatuletea matatizo.

Mheshimiwa Spika, tumeona kuna vihenge. Kuna mkataba wa ujenzi wa vihenge, kuna Mkataba wa Aurial ambayo ni kampuni ya Philips ambayo iko kule Uholanzi ya ku-supply vifaa vya tiba. Kuna mikataba mingi ambayo imetusababishia hasara ya fedha nyingi. Pia kuna mikataba mingine mingi ambayo hatujaiona, na labda baadhi ya wabunge hawajaiona.

Mheshimiwa Spika, tunayo pia mikataba ambayo tunatakiwa tulipe kama current liabilities, kama madai sasa ni trilioni 1.7 kwa TANESCO kutokana na kesi mbalimbali zinazotokana na uzalishaji wa umeme, usamabazaji na matumizi yake, ambako kuna kampuni tatu zinatutadai ikiwemo kampuni maarufu IPTL kupitia Standard Chartered Bank Hong kong.

Mheshimiwa Spika, Kwa hiyo ukingalia mikataba mingi ambayo tu nayo inatunyonya sana kuliko kutusaidia kama nchi, na inatumika kama conduit, ni kama vile tumechukua tenga tunaenda kubeba maji; ambazo ni fedha, halafu yanadondoka nje kwa sababu tu hatujaweza kuziba mianya kupitia mikataba.

Mheshimiwa Spika, wewe ni Mwanasheria na unafahamu uandaaji wa mikataba. Ni kesi chache sana ambazo Serikali imewahi kushinda kwenye mabaraza ya usuluhishi au Mahakama, kesi chache sana. Nafikiri wengi watakumbuka City Water ndiyo ambayo tumewahi kushinda, lakini kesi zingine zote tunashindwa, hata pale ambapo mwekezaji au mtoa huduma hajatimiza masharti yake lakini bado sisi tunashindwa kwenye hizo kesi na kulazimika kulipa mabilioni ya fedha za Serikali. Baadaye tunahangaika Kwenda tunaenda kukopa, kuweka tozo, kuwabana wajasiliamali wetu na kuwabana wafanyabiashara walipe kodi, pesa ambazo kimsingi tumeshindwa kuzilinda.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni manunuzi. Bahati nzuri Weheshimiwa wenzangu walizungumza hapa, akiwemo Mheshimiwa Maimuna Pathan na Mheshimiwa Deus Sangu. Upande wa manunuzi tunapoteza fedha nyingi, miradi mingi haiishi kwa wakati, ina extension na variations za kutisha.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu na mwaka jana tulipewa taarifa hapa kwamba hata ujenzi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere kufikia Novemba, 2021 ilitakiwa maji yaanze kuingia kwenye bwawa kwa miezi mitatu hadi minne na commission ingeweza kufanywa mwezi Juni, 2022. Hata sasa hapa tunavyoongea kuna extension tena ya miaka miwili sijui. Hatuelewi hiyo extension imetokana na nini na gharama ni nani analipa? Mapato ambayo tungepata kwa kuuza umeme nani atafidia? Hata kasi ya usambazaji wa umeme wa REA haiwezi kuwa kubwa kwa sababu kiwango cha umeme kinachozalishwa ni kidogo. Tulitegemea umeme huu ungeweza kuingia haraka kwenye grid. (makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaona pia kuna madhaifu ya kiutendaji. Kuna maeneo mengi tumeona ukusanyaji wa kodi umekuwa ni mdogo. Kuna changamoto katika ukusanyaji wa kodi.

Mheshimiwa Spika, moja, mfumo kupitia Tax admiration Act si mzuri sana; na kuna systems ambazo zinakadiria kodi kubwa kuliko uhalisia na pia kuna upungufu wa utaalamu. Wako wataalamu wa upande wa kodi hata mkopo wanaupigia hesabu ya capital gain tax, matokeo yake liabilities kwa wafanyabiashara inakuwa kubwa na hawawezi kulipa, wanahangaika, wanalazimika kufanya objection tunakwenda huko kwenye TRAB na TRAT mnakokusikia.

Mheshimiwa Spika, hii yote ni kutokana na kubadilika na mfumo wa kiutendaji ambapo zamani kulikuwa na a proper tax accessor ndani ya TRA ambaye amefundishwa, ame-undergo intensive training kule TIA au sehemu nyingine ya nchi, akiwa ni mtaalaamu wa ukadiriaji wa kodi kwa sababu amebobea kwenye eneo lile na ni mtaalamu. Sasa hivi mtu yeyote tu, akikaa kule Masasi ofisini au Kalambo anakukadiria tu. Jambo hili limepelekea tax disputes nyingi na objection kuzalishwa.

Mheshimiwa Spika, ningependa sasa kuchukua muda mrefu kujielekeza kwenye mapendekezo. Naomba Waheshimiwa Wabunge mridhie mapendekezo haya ili tuweke kwenye maazimio yetu kupitia Mwenyekiti wetu wa Kamati ya PAC.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, ninashauri; ili kuziba mianya ya mapato na matumizi ya Serikali, mikataba yote ambayo inazidi five bilioni iletwe bungeni kupitia kamati, au kamati maalumu tuweze kuihakiki na kui- approve.

Mheshimiwa Spika, la pili, mikataba yote iliyopo kwa sasa, najua kuna juhudi zilikuwa zinafanywa na Serikali kupitia mikataba mbalimbali kuweza kuihuisha, kuiboresha na kuifanya ya kisasa angalau kulinda maslahi ya watu wetu, nayo iletwe tuihakiki na kuiona kama mikataba hiyo ina maslahi na kama haina maslahi tukae mezani tuweze kuijadili upya tuweze kufanya review ya hiyo mikataba.

Mheshimiwa Spika, iko mikataba ya upande wa madini, gesi na upande wa kwenye vitalu vya utalii kule na maeneo mingine ya kimkakati. Iko miradi ya SGR, Stiegler’s gauge na upanuzi wa bandari. Tulienda Tanga, kule kuna vitu vya ajabu sana nafikiri na vingine mlivisikia, ambapo mtu amepewa tenda leo halafu kesho aka- subcontract kwa mtu mwingine kwa bei ya chini ya nusu ambayo analipwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, mimi napenda kushauri sana mikataba hii tuitishe upya, tuweze kuipitia na kuitengenezea frame work ili iwe mikata ambayo ina faida kwetu.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni la adhabu na tuzo ambazo zinatolewa kwenye taasisi za usuluhishi au mahakama za usuluhishi wa migogoro ya wafanyabiashara na wawekezaji. Iko ICC Internationa Chamber of Commerce pamoja na Ixid ICSID ambako kule tunashindwa mara nyingi.

Mheshimiwa Spika, mimi nilikuwa nashauri kabla ya Serikali haijalipa chochote huko sisi tutoe azimio, Serikali ije Bungeni tukae nao na tujadiliane nao tuone hicho kinachokwenda kulipwa ni nini, kina-make sense namna gani na kama kweli tunaridhia; ili fedha ya umma inapokuwa inatoka kule sisi kama wawakilishi wa wananchi basi tuwe na taarifa nayo.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo kubwa sana kwenye suala la ukusanyaji wa kodi. Tumeambiwa hapa zaidi ya trioni 2.8 hazijakusanywa. Ukiangalia zile sababu kutokana na taarifa za CAG zinaonesha kwamba mfumo wa kodi wa sasa umepitwa na wakati. Aliyekuwa Waziri wa fedha wakati ule ambaye kwa sasa ni Makamu wa Rais, Mheshimiwa Philip Mpamgo, aliwahi kutoa mapendekezo kwamba kuna Presidential Recall Committee on Tax Systems Reforms ambayo ilifanywa mwaka 1992 chini ya Mzee Mtei na haijawahi kufanywa tena. Ili tuweze kuona fiscal policy yetu ikoje, nani tumtoze, vyombo gani, tuendelee na VAT ya asilimia 18 ilhali wenzetu ni asilimia 16 kwenye kanda. Je, mfumo wa TRA upoje? Je, bado ibaki kama ilivyo? Au idara za TRA zibaki kama thematic departments.

Mheshimiwa Spika, kwamba kama Idara ya VAT iwe Idara ya VAT, na isiwe inafanya tax payer na kufanya VAT, Domestic revenue anakusanya VAT hii inaleta mkanganyiko mkubwa sana. Kwa hiyo nilikuwa naomba sana waheshimwa Wabunge tukubaliane, kwamba tuiagize Serikali kama maazimio iweze kufanya comprehensive tax system review ili tuweze kubaini mfumo wetu wa kikodi ukoje ili tupate kodi za kutosha.

Mheshimiwa Spika, hii itatusaidia kuongeza tax effort. Tax hatujilipii ratio ambayo kwa bahati mbaya tangu mwaka 1995/1996 bado tuko asilimia 10 hadi 11. Maana yake ni makusanyo yote ya kodi kulingana na uzalishaji (tax over GDP) ambayo tuko below African average ya asilimia 18. Hii naamini itatusaidia kutengeneza mfumo mzuri na kuitengeneza compliance kubwa, watu walipe kodi wakiwa na furaha kwamba wanachangia kwenye maendeleo kwenye taifa lao.

Mheshimiwa Spika, kuna hii tabia ya Serikali kukaa na fedha za wafanyabiashara kwa sababu imeshindwa kulipa kwa wakati kutokana na zabuni au ukaguzi wa imports duty na refunds. Mimi ninasema, kama Serikali inatoza faini na penalties kwa mfanyabishara kuchelewa kulipa fedha Serikalini basi sasa kwa uwajibikaji Serikali nayo ijitoze faini na riba kwa mfanyabiashara endapo tutachelewesha malipo kwao. Kwa sababu tunachelewesha malipo kwao tuna-hold working capital zao; hili linasababisha ku-paralyze private sector.

Mheshimiwa spika, nilikuwa natamani sana, tumeliangalia sana shirika la TANESCO. Shirika la TANESCO lina mzigo mzito ambao umetokana na mfumo uliopo sasa hivi. Napendekeza tufanye upya mapitio ya Sera ya nishati ya umeme ili tufanye divestiture ndani ya TANESCO. Tunajua TANESCO inajihusiha na masuala ya uzalishaji, usafirishaji pamoja na usambazaji wa umeme, lakini tumeruhusu independent power producers kwenye uzalishaji peke yake halafu wanalazimika kumuuzia TANESCO. Kwa hiyo TANESCO hata kama hajajiandaa analazimika kununua na kuingia power purchases agreement na kutengeneza mzigo mkubwa ambao TANESCO sasa hivi tunauona.

Mheshimiwa Spika, mapendekezo yangu, kama ambavyo ilikuwa TTCL zamani tukaruhusu Vodacom, Tigo na wengine waingie, tufanye divestiture, turekeboishe sera zetu ili turuhusu na wengine waje wawekeze. Kama ni Symbion aweke mtambo wake azalishe, asambaze umeme wake, atafute wateja wake aendelee ili TANESCO iendelee kubaki salama kutokuingiziwa mzigo mzito kama ambavyo ilivyo hivi sasa.

Mheshimiwa Spika, tumeona pia suala la bodi ya mikopo. Mimi ningependa kuungana na Mheshimiwa Japhet Hasunga, alitoa pendekezo hapa jana. Napendekeza Serikali angalie uwezekano wa kuunda mfuko wa taifa wa kugharamia elimu ya juu na si bodi ya mikopo; ambao na utakuwa ni mfuko wa pamoja. Watoto wote wa Tanzania wanastahili kusoma.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano mmoja, nilipata bahati kipindi fulani kwenda kusoma Kijerumani CDTC center pale Koloni (Cologne) Ujerumani; tukawa na watoto wadogo kama 20 hivi tunasoma nao pale. Nikawauliza, walikuwa wanaongea kifaransa, wale Watoto wanatokea nchi ya Gabon. Serikali ya Gabon imetengeneza utatibu kwamba, kila mwaka the best science students form six wanapelekwa Ujerumani kusoma electrical engineering, mechanical engineering, civil engineering kwa gharama za Serikali for Seven-years, kila mwaka. Gabon haitakuwa sawa sawa na sisi baada ya miaka 20. Kwa nini sisi tuone hasara kuwasomesha watoto wote? Kwa nini tulazimike kumbagua huyu, sjui mzazi wake yukoje, mzazi wake hana mguu mmoja kwa hiyo tumpe.

MheshimiwaSpika, mimi ninapendekeza tuanzishe mfuko wa taifa, tutafute vyanzo, vyanzo vipo ili kila mtoto aweze kupata elimu.

Mheshimiwa Spika, tuna tatizo kubwa sana la Local content ambalo jana hata Mheshimiwa Kigwangala alilizungumza. Ni namna gani tutawawezesha watu wetu? Tunafurahia sana kuona orodha ya mabilionea wa nchi nyingine? Tunatakiwa sasa kuwatengeneza wa kwetu, tuwaamini wafanyabiashara wetu tuwatafute tuwatengeneze.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri sana Serikali ije na Local content law ili tuweze kupitisha hapa tukainisha maeneo mbalimbali ambayo tunaamiani tunaweza kuwasaidia Watanzania wetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, napenda kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
WAZIRI NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (UWEKEZAJI): Mheshimiwa Spika, kabla sijaanza kuchangia ningependa kukukumbusha kwamba siku mbili/tatu zilizopita kulikuwa na mechi kule Egypt na hujatuambia matokeo yake. Labda utatupa taarifa ukipata nafasi. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwanza ningependa sana kushukuru michango ya Waheshimiwa Wabunge, kwa kweli ni michango ambayo imesaidia sana kutengeneza Mpango wetu wa Miaka Mitatu ambao ni Mpango wa Tatu wa Maendeleo; na kwa kweli michango yenu tumeichukua na tutahakikisha kwamba tunaifanyia kazi kwenye maeneo yetu ya kisekta, lakini pia kuboresha huu mpango.

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba uniruhusu niwataje baadhi ya Waheshimiwa Wabunge ambao wamechangia kwenye eneo la uwekezaji. Kulikuwa na Mheshimiwa Zuberi Kuchauka (Mbunge wa Liwale), Mheshimiwa Tarimba Abbas (Mbunge wa Kinondoni); Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa (Mbunge wa Biharamulo) pamoja na Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani (Mbunge wa Viti Maalum Ruvuma). Pia kuna Mheshimiwa Hassan Mtenga (Mbunge wa Mtwara Mjini); Mheshimiwa Simon Songe na Mheshimiwa Yahya Mhata, huyu wa Nanyumbu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kushukuru kwa michango yao lakini naomba nijielekeze kwenye kuwahakikishia Waheshimiwa Wabunge lakini pia na wananchi kwa ujumla, kwamba Serikali wakati wote imekuwa ikifanyakazi ya kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara kwenye nchi yetu. Kama ambavyo mtakumbuka Waheshimiwa Wabunge mwaka 1999 tulikubaliana kwamba tuunde Dira ya Maendeleo ya miaka 25 (2000 – 2025), tunaiita Tanzania Development Division 2025 ambayo ilianza mwaka 2000, mwaka uliofuatia. Tukawa na mipango midogo midogo ya kimkakati sasa kutekeleza ile Dira ya Maendeleo; na ni kwenye ile dira tulijipangia kwamba mpaka kufika mwaka 2025 tuingie kwenye uchumi wa kati, lakini pia tukiongozwa na sekta binafsi, lakini pia na tukiongeza uzalishaji wetu wa mazao kwa ajili ya kupeleka fedha nje, tuwe na fedha za kigeni nyingi. Pia shilingi yetu iweze kuwa imara, tuwe na mfumuko (inflation) ya single digit, ikiwezekana twende kwenye chini ya wenzetu kwenye eneo la Afrika Mashariki na SADC na tukajipangia mipango mingi ikiwemo kukuza ajira kwa vijana; sasa tunakuwa na mkakati midogo midogo ya kuweza kutekeleza hivyo.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna reforms ambayo ndiyo nilitaka iwe hoja yangu kubwa. Kwamba tunafanya maboresho kila wakati kama Serikali kwa kupokea mawazo kutoka kwa wadau, lakini pia watekelezaji wa programu mbalimbali za kisekta. Kama mtakumbuka tulikuwa na Public Sector Reform Program ambayo iliunda Idara yetu ya Utumishi kipindi kile, lakini pia kuna Public Finance Reform Program, pia tulikuwa na Local Government Reform Program ambayo tumetengeneza hizi halmashauri kupitia hizo programu. Pia hata Legal Sector Reform Program tuliifanya wakati huo ili kuboresha sheria zetu ziendane na mahitaji yetu sisi ya kuwa na uchumi wa kisasa kuendana na malengo ya kwenye Dira ya Maendeleo.

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye kuyafanya hayo tukatengeneza mikakati. Tulikuwa na mkakati mdogo wa miaka mitatu wa kupunguza umaskini lakini tukasema huu mkakati baada ya kupata maoni ya wadau tuupanue zaidi kwa kukuza uchumi na kuupunguza umaskini. Tulikuwa na MKUKUTA, MKUKUTA I na MKUKUTA II wa miaka mitano, mitano kama mtakumbuka. Kwenye MKUKUTA II tukaona sasa tuje na mpango tofauti kidogo, ndipo tukawa na huu Mpango wa Maendeleo ya Miaka Mitano ambao Mheshimiwa Rais wetu wa Awamu ya Nne Dkt. Jakaya Kikwete alizindua mwaka 2011/2012 mpaka 2015/2016 mpango wa kwanza ukilenga kuibua fursa za kiuwekezaji lakini pia kujenga miundombinu ili tuhakikishe kwamba tunajenga msingi mpana wa kukuza uchumi wetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kutekeleza huo mpango tukaja na mpango wa pili sasa wa miaka mitano mingine ambayo ni 2016/2017, 2020/2021 ambao ndiyo umekamilika, huu tukasema tujikite kwenye ujenzi wa viwanda, na ndiyo maana Serikali inaripoti mara kwa mara kwamba tumejenga viwanda zaidi ya 8,477 ambako vikubwa ambavyo tunaviona ni 210 kwenye nchi yetu, ambavyo vimetoa ajira za kutosha kwa vijana wetu, lakini kutengeneza mafungamano kati ya sekta ya kilimo na masoko kwa kuwa na viwanda katikati ili tuweze kuchakata bidhaa za wakulima, lakini pia kutengeneza immediate market (soko la karibu) la mkulima na kumuhakikishia mkulima soko la mazao yake.

Mheshimiwa Spika, lakini pia sisi kama nchi tukasema baada ya kupata mafanikio kwenye Awamu ya Kwanza na ya Pili ya Mipango ya Maendeleo kupitia Long Term Perspective Plan sasa twende kwenye Mpango wa Tatu ambao unaishia 2025/2026 na huu mpango umejikita kwenye ku-consolidate na kuchukua yote yale ya nyuma, lakini pia na kuchukua yale ambayo hatukuweza kuyatekeleza au kuyaboresha ili tuweze kwenda mbele. Sasa kwa upande wa uwekezaji kuna mengi ambayo tumeyaona kuna mafanikio makubwa sana ambayo sana tumeyapata kipindi hiki cha miaka iliyopita kutekeleza Mpango wa Miaka Mitano wa Kwanza na wa Pili.

Mheshimiwa Spika, lakini kwenye Mpango wa Tatu tumelenga kuongeza; moja, utekelezaji wa mipango ya kuboresha mahusiano yetu sisi na sekta binafsi na tutaongea hizi PPDs (Public Private Sector Dialogue) kwa kuwasikiliza zaidi wafanyabiashara.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili kuweza kuboresha complaints handling; zile kero za wafanyabiashara zile tuwe na masikio mapana zaidi ili tuweze kuzisikia na kuhakikisha kwamba tunatekeleza yale ambayo wafanyabiashara wangetamani, kwa sababu wao ndio wazalishaji na wasambazaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kipindi hiki tunasema blue print ambayo imezungumzwa hapa tunaenda kuitekeleza kwa uhakika labda niseme hivyo. Tangu mwezi Mei, 2018 baada ya Baraza la Mawaziri kuridhia na pia ndani ya Serikali kuweza kuhamasisha wananchi uwepo wa blue print na wafanyabiashara tumeweza kutekeleza mambo mengi ikiwemo kupunguza tozo 273 kwenye eneo letu la kujenga mazingira ya biashara na uchumi. Lakini pia kama mnakumbuka tulikuwa na TFDA ambayo ilikuwa inafanyakazi ambazo zinagongana kidogo na TBS. Kwa hiyo, Serikali baada ya kupata ushauri kutoka kwa wadau ikiwemo Waheshimiwa Wabunge hapa Serikali ikaamua kuchukua eneo la chakula na vipodozi ikapeleka TBS na kuiacha TFDA kushughulika na madawa na vifaa tiba ndiyo maana inaitwa TMDA kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutajitahidi sana kuhakikisha kwamba tunatekeleza mipango yetu ambayo tumejiwekea kupitia blue print, lakini pia na maboresho mbalimbali ambayo tulianza tangu mwaka 2010 kupitia ofisi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunaita maboresho, ambayo imetokana na kufuatilia na kutafiti juu ya ripoti ya IFC ya Benki ya Dunia ya Easy of Doing Business, kuna indicators kumi na moja ambazo zinatuonesha hatufanyi vizuri kulinganisha na nchi zingine duniani. Kila nchi inapigana na kukimbia kwahiyo tutajitahidi kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba tunatekeleza hiyo yale maboresho na kuwa na mazingira wezeshi zaidi.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nipende kusema tui le miradi mbalimbali ya kimkakati ambayo imelengwa kufanywa na Serikali itafanywa ikiwemo Mradi wa Bagamoyo ambao Mheshimiwa Engineer Ezra Chiwelesa ameulizia. Serikali iko wazi kwenye hilo kwamba tulichokataa ni yale masharti tu ambayo hayakuwa mazuri sana kwa nchi yetu, lakini kwa kweli wakija tena wale wawekezaji au wakitokea wengine tukakaa chini tukaongea tukaja na masharti ambayo yana interest kwa nchi, Serikali haitapinga kwa sababu ule mradi ni wa kwetu Serikali, wala si wa wawekezaji ni wa kwetu sisi. Na kwa kweli hayo maeneo mbalimbali tumeshalipia fidia sehemu ya viwanda, sehemu ya logistics lakini pia na sehemu ya bandari tumelipia fidia kabisa yako chini ya mikono ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ningependa kuwahakikishia Wabunge na kuwahakikishia wafanyabiashara jumuiya ya wawekezaji kwenye nchi yetu, kwamba Serikali itaongeza usikivu na kuhakikisha kwamba tunafanya kazi pamoja kuweza kuboresha mazingira ya biashara.

Mheshimiwa Spika, napenda kukushukuru sana na naunga mkono hoja.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi hii ili niweze kuchangia machache kwenye Mapendekezo ya Mpango wetu wa Maendeleo, ambao utaenda kutafsiri mpango wetu wa bajeti wa mwaka wa fedha 2023/2024. Kutokana na ufinyu wa muda, naomba niende haraka haraka. Kwanza, nataka kupendekeza, Mpango huu, ukiuangalia na ukiusoma ni kama academic paper. Ni mpango ambao unatengeneza matarajio na tamaa tuliyokuwa nayo. Tumetohoa kutoka kwenye Mpango Mkuu ule wa Miaka Mitano ambao ni mpango wa mwisho kabisa katika kutekeleza Dira ya Maendeleo ya mwaka 2000 - 2025.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu kwamba Dira ya Maendeleo inaisha 2025 na huu Mpango wetu una-overlap kwenda 2026. Kwa hiyo, ni lazima tuwe na mipango ambayo tutakuwa tunajitathmini kila wakati katika kutengeneza ule mpango wa mwisho kabisa. Sasa nimesema kwamba kwa jinsi ambavyo unaonekana ni kama vile tumeorodhesha tu tunachotamani kiwepo, lakini kimsingi hauoni ule mpango ndani ya Mpango huu. Sasa napenda kupendekeza yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kuweza kutengeneza malengo mapana zaidi, hapa malengo yapo matano tu na ukiangalia yote ni macro-economic objectives. Kwa hiyo, tumefinya mpango huu kwenye kutaka ku-achieve only macro-economic objectives na wakati mpango mpana ule tumesema tupate competitive and industrial economy for human development. Kwa hiyo tuna mambo matatu pale, tuna competitiveness, industrial growth, lakini pia kuna human development.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilitegemea kwenye malengo makuu yajigawe katika maeneo yote matatu lakini ukiangalia pia imejifinya kabisa, ni maeneo matano tu ya ukuaji wa uchumi, Pato la Taifa, tax effort, tax to GDP ratio, imejifunga kwenye maeneo matano tu. Kwa hiyo, naomba tupanue twende kwenye maeneo mengine ambayo yanagusa wananchi. Kwa mfano, tunafahamu Ilani ya Uchaguzi ya CCM ambayo imekuwa referred humu kama moja ya reference documents. Inasema ni lazima tutoe ajira kwa vijana kufikia milioni nane mwaka 2025, lakini kwenye mpango huu huoni mwaka huu kwamba tutatengeneza ajira ngapi? Sasa hivi itatuonyesha tu jinsi ambavyo Serikali kuu itaajiri, sijui vibali vya ajira 32,000, sijui na nini, lakini haifanyi mirroring kwenye Mpango Mkuu wa Miaka Mitano, tukijikita kwenye maeneo yale ambayo tumejiwekea sisi kama Taifa kama malengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo napenda kabisa kwenye Mpango huu tuonyeshe waziwazi, kwa mwaka huu tutatengeneza ajira ngapi za vijana wetu? Mwakani tukifika, ajira ngapi? Kufika 2025 twende tumesema kwamba okay, hizi indicators ni measurable, tumeweza kuzi-achieve na kwa kweli tumetekeleza wajibu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tumesema tunataka tutanue wigo wa kodi, lakini ukisoma document huoni kwamba tutatoka kwenye tax GDP ratio ya 11.7 kwenda 12 kwa kutumia njia zipi? Je, kutakuwa na mfumo mpya wa kodi? Pili, tutatengeneza compliance mpya ya kikodi? Tatu, tutatengeneza mazingira rahisi zaidi ya kikodi? Nne, existing taxpayers watatengenezewa utaratibu wa kulipa vizuri zaidi, tutaenda kwenye TRAB na TRAT kule kwenda ku - resolve zile disputes nje ya mahakama au tutaenda kutengeneza taxpayers wapya ambayo ni walipakodi binafsi kama personal income taxpayers au corporates, tunaenda kuzalisha walipa kodi wapya kwa kutumia njia ipi, hatuoneshi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango mpana unasema tutakuza eneo la utaalam wa watumishi wetu. Sasa hatuonyeshwi hapa ule utaalam wa watumishi wetu ambao tunalazimika kutoa vibali vya kazi kwa wafanyakazi kutoka nje ya nchi, tunaziba vipi ile gap? Tumeambiwa kwenye Mpango Mkuu hata kwenye ile preface ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, anasema kabisa pale, tutakwenda kutengeneza wataalam kwenye maeneo mbalimbali ambayo yanahitajika ku-respond to the market demand, lakini ukiangalia hapa huoni kwamba mitaala yetu itaendelea kubaki vile vile au itabadilishwa na kama itabadilishwa, itabadilishwa nini? kwa sababu mpango lazima useme, tunaenda kubadilisha nini ili sector ministry iwajibike kupitia Mpango huu. Huu Mpango ni Mpango Mama, lakini huioni hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa natamani kuona kilichoandikwa kwenye Mpango Mkuu kinatafsiriwa moja kwa moja huku. Kwa mfano, tumesema reli ya kutoka Mtwara kupitia Masasi kwenda Songea na Mbamba Bay pale Ziwa Nyasa na kuwa na branch spur kwenda pale Liganga na Mchuchuma pale Ludewa, ambayo baadaye tumesema tuta-connect pia kwenda Makambako kuingia kwenye TAZARA. Huo mpango tumeandika kwenye Mpango wa Miaka Mitano kwamba utatekelezwa under PPP program, lakini kwenye mwaka huu haijaoneshwa kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tafsiri yake ni kwamba tunasubiri miaka mitatu iliyobakia labda huko ndio tutaonyesha kama mpango. Kwa hiyo, naomba wenzetu wa Wizara ya Fedha waionyeshe hiyo kama ni mpango ambao tunaanza nao mwaka huu, tuta-attract expression of interests waweze kuja, kama tunavyofanya kwenye hizo EPC+F kwenye maeneo ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitarajia pia sekta za uzalishaji, of course, sifurahii sana kuona kwamba kwenye mchango wa Taifa wa GDP, sekta ambazo zinaongoza ni sekta ambazo, Sanaa na Utamaduni, sijui Habari, Sekta za Uzalishaji za Kilimo, Mifugo, Uvuvi, Viwanda zipo chini kabisa. Kwa hiyo, nafikiri mpango huu ungeweza kusema. Tuna Viwanda kwa mfano 11 vya Ubanguaji wa Korosho, vikiwemo vya pale Masasi ambavyo ni vikubwa kuliko viwanda vyote pale. Hivi viwanda havifanyi kazi na korosho sasa hivi tumesikia hata bei ya korosho ni chaos kule kwetu, bei sasa hivi imetoka shilingi 4,000 kwenda shilingi 1,400 mpaka shilingi 1,800.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna mpango gani kwenye mwaka huu tuhakikishe kwamba viwanda vyote vya korosho, vya pamba, vya alizeti, vya nini, vitafanya kazi, tuna mpango upi ambao tutaonyesha humu? Ni vizuri tuonyeshe ili ikifika mwakani tunajipima kwamba kweli intervention yetu imefanya kazi. Kwa hiyo, tunakuwa na indicators ambazo kweli zinaonyesha sisi tunawajibika. La si hivyo tutajikuta tunakuwa na natural growth ambayo ilizungumzwa na Mheshimiwa Magessa asubuhi. Ule ukuaji mdogo mdogo wa asilimia 0.2 ile ni natural growth ni ukuaji wa asili. Whether umefanya kazi au hujafanya, umepanga hujapanga, utakua tu, kwa sababu watu lazima wazalishe, lazima wale lazima wanywe. Kwa hiyo, kuepuka hiyo ili tuonekane na sisi tumefanya kazi yetu vizuri, tutengeneze a planned growth ambayo tutakuwa na growth kama za wenzetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia natamani sana, eneo ambalo tumeligusa na humu limezungumzwa kuboresha huduma za watumishi wa umma kwenye jamii. Tunaboreshaje? Haisemi! Nina mawazo na nikuombe kweli, hili Bunge letu lazima tufikirie, umefika wakati na hata ukiangalia ripoti za CAG, ile ya PAC na LAAC lakini pia PIC ambayo tumejadili wiki iliyopita. Tumeona kuna laxity kubwa kwenye Public Service Management. Watumishi wa umma wame-relax kabisa kwa sababu tu wana security ya kazi zao. Kumfukuza mtumishi wa umma ni shughuli kweli kweli, natamani kweli kwa sasa hivi tumefikia wakati wa teknolojia, tuwe na utaratibu wa mikataba...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante, kengele ya pili hiyo.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE:…kwa watumishi wa umma ili anayefanya vizuri tumpandishe, anayefanya vibaya aondoke, apishe nafasi kwa watu wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Napenda kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Kwanza kwa niaba ya watu wa Masasi ningependa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutufikisha siku ya leo. Pia nikishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kinachoongozwa na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutupigania Watanzania lakini kipekee kwa kunipigania mimi Mbunge wao kule Masasi kwa kuhakikisha kwamba changamoto za Masasi zinaondoka. Na Masasi sasa hivi ni mpya, na kila mmoja anaiona kwamba Masasi inang’ara. Hiyo yote ni juhudi za Mheshimiwa Rais kuniunga mkono mimi kama Mbunge wake tukishirikiana na Mheshimiwa Madiwani ambao niko nao kule Masasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo ningetamani nichangie kwenye bajeti hii ambayo imewasilishwa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango. Tunafahamu kwamba bajeti ni makadirio ya mapato na matumizi, ni makadirio tu. Kwa hiyo nina michango kwenye maeneo haya mawili; mapato na matumizi. Ningeomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha anisikilize, najua itamsaidia. Na kwa sababu muda ni mdogo nitajitahidi kwenda haraka haraka. Yeye ni mchumi mwenzangu, anajua, kwamba nikizungumza kitu basi ajue namna ya kuki-pick.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, na hii naendelea kusisitiza sana; any sense to the government, the first concern ni employment ya vijana wake. Tukitengeneza fursa pana za ajira kwa vijana tafsiri yake tunaongeza direct tax payment. Kwa upande wa wale vijana wanalipa kama pay as you earn, ambayo ni personal income tax kutoka kwenye mishahara yao lakini pia makampuni na shughuli watakazokuwa wanazifanya nazo zinalipia cooperate income tax, ambayo ni direct tax ambayo ni ya uhakika kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukifanya hivyo tunaweza tukahakikisha kwamba tunatoa fursa pana zaidi kwa Serikali kukusanya kodi ambayo inaweza ikasaidia kwenye upande wa matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inaendana na adhma ya kupanua tax base. Amezungumza Mheshimiwa Kihenzile hapa inasumbua kidogo; na bahati nzuri nilihudumu kidogo kwenye Bodi ya TRA. Tunaolipa kodi ni wachache sana kwenye nchi hii. Sensa imeonesha kwamba tuna watu milioni 61 lakini walipa kodi hapa ni kama milioni tatu tu wale wenye active TIN Number, wako milioni tatu tu; na hiyo ni watu binafsi pamoja na kampuni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo ni watu wachache sana wanaolipa kodi, matokeo yake concentration inakuwa kubwa kwa sababu wachache wanaolipa kodi wanalazimika kulipa kodi sana na wanalazimika kukamuliwa sana ili kufikia malengo ya kitaifa, lakini tungetanua tax base tungerahisisha na kufuata zile rules tano za usimamizi wa kodi. Kwamba kodi lazima kuwe na fairness, kodi lazima kuwe na adequacy, kodi itoshe kuitosheleza Serikali lakini kuwe na simplicity, kuwe na urahisi wa ulipaji kwa yule mlipa kodi kwa sababu ya compliance iko juu lakini lazima kuwe na transparency la mwisho lazima administratively kuwe na easiness, kuwe na urahisi wa kukusanya hizo kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa natamani nigusie kwenye maeneo ambayo tunaweza tukasaidia hawa vijana kupata ajira nyingi pia tupate kodi za kutosha. Eneo la kwanza; tunafahamu kuna ule mradi wa Mkurabita nchi yetu sisi structure ya uchumi wetu asilimia 60 mpaka 70 ni informal sector, kule kodi huwa hazipatikani kirahisi kwa sababu si sekta rasmi. Kwa hiyo Mkurabita nafikiri imeshakufa. Lengo kubwa lilikuwa ni kuweza kutengeneza utaratibu wa kampuni mbalimbali na watu binafsi shughuli zao ziweze kurasimishwa ili waingie kwenye tax net waweze kulipa taxes kwa kuwa tax payers. Kwa hiyo nilikuwa nafikiri Mheshimiwa Waziri arudi kwenye ku-reform informal sector ili ziwe formal kupitia mikakati mbaliambali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, mwaka wa jana Bunge lako Tukufu Mheshimiwa Mwenyekiti lilipitisha azimio kutoka kwenye Kamati yetu ya PAC la ku-undertake a comprehensive tax system regime of view ambayo ilifanyika mwaka 1992 ambayo ndiyo iliyotengeneza mifumo ya kuanzishwa kwa TRA. Kwamba ni structure ya aina gani ya kodi tulipe, nani alipe, aina gani ya shughuli zitozwe na viwanda vikoje. Yaani tupitie upya huo wigo mzima wa kikodi ili tuhakikishe kwamba tunapata walipa kodi sahihi aina ya kodi sahihi pia na mfumo wa ukusanyaji ambao uko wezeshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ni uwajibikaji wa wizara zingine zote za kisekta kumsaidia Waziri wa Fedha kukusanya mapato, kumsaidia kutengeneza mapato. Kazi ya wizara hizo ni kutengeneza vyanzo vya mapato kwa ajili ya Wizara ya Fedha. Kwa hiyo kila Wizara ingetakiwa kuwa na lengo inayopewa iwe ni four trillioni, wewe five 5 trillion, wewe three trillion. Wakae na kuona; yale maeneo ambayo Waziri wa kisekta ana changamoto nayo anamwambia Waziri wa Fedha ili nikuletee four trillion naomba labda 10 billion kwenye eneo hili. kwa mfano Mheshimiwa Waziri Bashe anaweza kabisa kuweka mkakati wa kufufua viwanda vya korosho kule Masasi, Tunduru, Lindi na kwingineko; ili ajira zikiwa nyingi pamoja na kuongeza thamani kodi inakuwa ni kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunafahamu kwamba tuna mradi mkubwa wa Mtwara Development Corridor ambao unatakiwa kuchochea kule ikiwemo Liganga na Mchuchuma pamoja na ujenzi wa ile reli ya kule Kusini. Tukifanya hayo na matumizi sahihi ya Bandari ya Mtwara tutakuwa na trilioni ya fedha ambazo tutazikimbia. Lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kwa kusema naunga mkono hoja asilimia 100 na sisi watu wa Masasi tuko Imara kuweza kuhakikisha kwamba tuna-support Chama cha Mapinduzi kiweze kupata maendeleo, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza napenda kuunga mkono hoja za Wenyeviti wa Kamati zote tatu ambao wamewasilisha hapa Bungeni siku ya leo. Hata hivyo, naomba nichangie kwenye baadhi ya maeneo nikiwa kama Mjumbe wa Kamati ya Hesabu za Serikali PAC.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba jukumu tulilonalo kama Bunge ni usimamizi wa Shughuli za Serikali ikiwa ni pamoja na kushauri pale ambapo panawezekana. Kwa hiyo, naomba niwe na maeneo ya kushauri kutokana na observations ambazo nitazifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujikita zaidi kwenye taarifa iliyowasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Hesabu za Serikali kutokana na ufinyu wa muda ili angalau niwe na mchango fulani wa kutoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwenye nchi yetu na bahati nzuri Waheshimiwa Wabunge wenzangu wamezungumza hapa, kwamba tuna kiu kubwa ya maendeleo kwenye nchi yetu. Pia, tuna changamoto kubwa sana ya ajira kwa vijana. Vijana tunao wengi na tuliahidi kwenye ilani CCM kwamba tutatengeneza ajira zisizopungua milioni nane kufikia mwaka 2025. Hata hivyo, tumejiainisha kupitia Ilani ya CCM kwamba tutaenda kutoa huduma kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya yote ambayo tumeyafikiria na tumeyapanga yatawezekana tu kama maeneo mawili makubwa ndani ya Serikali tutaweza kuyafanyia kazi. Kwanza ni kutengeneza mapato ya kutosha. Kuhakikisha kwamba tunakuwa na mapato ya kutosha kwa Serikali yetu kuweza kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo ni la msingi pia ni kudhibiti matumizi yasiyo sahihi na kuchukua hatua kali kwa wote ambao wametumia vibaya fedha za Serikali. Sasa nataka niguse maeneo machache tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la kwanza ni kuhusiana na miradi ya maji ambayo imekaguliwa. Mwenyekiti wa Kamati amezungumza hapo kwamba kuna matatizo makubwa ambayo tumeyaona ndani ya miradi ya maji. Hii ipo kwenye eneo pana la utambuzi wa mradi, designing ya mradi na utekelezaji wake. Inaonekana kama hatuna National Water Supply Master Plan. Ni kama tunabahatisha tu kulingana na vyanzo vidogo vidogo ambavyo tunavipata kwenye maeneo ili tu-address tatizo kwenye maeneo kule. Matokeo yake tunajikuta tunatumia fedha nyingi za Serikali kufanya miradi midogo midogo ambayo siyo endelevu, na hata mingine inapelekea kuwa chanzo cha uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napendekeza kwamba tuwe na Master Plan ya Kitaifa, tuainishe vyanzo vikubwa, vichache, na tupeleke fedha kwa ajili ya kwenda kuibua miradi ile mikubwa na kusambaza maji kwenye maeneo yote kupitia miradi mikubwa kuliko miradi hii midogo midogo ambayo tunatumia pesa nyingi ambayo siyo endelevu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, tuna Bwawa la Mwalimu Nyerere, lakini pale chini tuna Kijiji cha Mlalo, Lower Rufiji, maji yanapoelekea Baharini kutoka kwenye Bwawa, ni maji ambayo tayari yameshatumika kwenye Bwawa. Designing ambayo inafikiriwa kufanyika sasa hivi ni kutoa maji pale, kupeleka Kibiti, Ikwiriri, Mkuranga Dar es Salaam.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tulifikiri kwamba ilitakiwa ifanyike comprehensive designing ili kuwe na Northern Circuit au Northern Zone na Southern Zone ili maji yale ya Bwawa la Mwalimu Nyerere pia yaweze kuelekezwa kwenye Mikoa ya Lindi na Mtwara, ili kuhakikisha kwamba tunatatua kabisa tatizo la ukosefu wa maji Lindi na Mtwara, kwa sababu tu tunacho chanzo cha uhakika wa maji kwa upande wa Rufiji. Kwa hiyo, tukifanya hivyo itatusaidia sana kupunguza gharama na pia kuwa na vyanzo vya uhakika vya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile miradi mingi imetekelezwa ikiwa na variations nyingi. Tunalazimika kulipa fedha nyingi kutokana na usimamizi mbovu na uwajibikaji mdogo wa watumishi wa umma kusimamia hii miradi. Hii tumekuwa tukiizungumza sana na kwa kweli labda tujaribu kufikiria kama Bunge.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika maswali yetu ambayo tulikuwa tunawahoji hata Maafisa Masuhuli, tulikuwa tunawauliza, hii business as usual, comfort zone ambayo watumishi wa umma wanayo na kinachoitwa security kwa watumishi wa umma kwamba huwezi kufukuzwa kazi kirahisi ndani ya Serikali, tuendelee nayo au twende kwenye ajira za mikataba ambayo ni performance based? Kwamba ukisababisha hasara kwa Serikali, unaondoka. Kuliko ilivyo sasa wako kwenye comfort zone, kumfukuza mtumishi ni kazi ngumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tuliangalia eneo la uingizaji wa mapato. Kwenye kuingiza mapato, tuliangalia eneo la utalii, bahati nzuri Mheshimiwa Vuma amezungumza hapa, ingawa tutatofautiana naye kidogo kwa jinsi ambavyo tulikuwa tumeona sisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kufanya mahojiano na watu wa utalii wakiongozwa na Afisa Masuhuli wa Wizara ile, tulibaini kwamba hawana mkakati wa wazi wa kukuza utalii kwenye eneo letu. Pia kuna ushirikishwaji mdogo au uratibu mdogo ndani ya Serikali na sekta ya utalii na sekta nyinginezo ambazo shughuli zao kwa namna moja au nyingine zinaathiri shughuli za utalii. Kwa hiyo, tulikuja kuona kwamba hata wakiomba bajeti, unawapa kwa ajili ya kazi ipi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, Tanzania ni ya pili baada ya Brazili kwa kuwa vivutio vingi vya utalii; kuanzia utamaduni (culture), mpaka vivutio vyenyewe vya kwenye mbuga. Tuna kila kitu; ukienda kwenye beach tourism, kwenye kila kitu, lakini idadi kubwa ya watalii ambayo tumewahi kuipata ni watu milioni moja laki tano sijui na ishirini na mbili elfu sijui na ngapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni idadi ndogo mno ukilinganisha nchi kama ya Ufaransa ambayo imeweza kuingiza watu milioni 89.4 kwa mwaka; ukienda Hispania imeweza kuingiza watu milioni 83.7 kwa mwaka; ukienda Marekani milioni 79.3 kwa mwaka ambao hawana kabisa vivutio kama tulivyo navyo sisi, lakini wameweza kuvutia watu mamilioni kwa mamilioni. Sisi tumevutia watu milioni 1.5, tena hao milioni 1.5 kuna double counting humo ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna conference tourism. Kuna watu wanakuja tu kwenye mikutano ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, wanahesabika kwamba ni watalii. Wanakuja kwa ajili ya mikutano ya SADC, wanahesabika kama ni watalii. Sasa hivi JKCI tunatibu watu. Watu wanatoka Malawi wanakuja kutibiwa pale JKCI Muhimbili, nao tunawahesabu kwamba ni watalii. Ni watalii wangapi wametokana na mipango hasa ya Wizara ya Utalii na implementation yake katika eneo hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni maeneo ambayo tungeweza kuingiza fedha za umma ambazo siyo za kikodi (non-tax revenue). Ni public asset ambayo tunayo na hatuitumii. Kwa kweli tunasikitika kwamba tunavyo vyanzo kabisa vya kuweza kuingiza fedha, lakini hatuvitumii kuingiza fedha. Hii inapelekea pressure kubwa kwa Waziri wa Fedha, inabidi ahangaike kutafuta mikopo. Mikopo ya sasa hivi, concession loans zinapungua na non-concession zinaongezeka, ambapo baadaye tutakuja kutengeneza burden kubwa katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile tuna vyanzo vya uhakika vya kuongeza fedha ambazo ni non-tax revenue ambazo ni za kwetu. Mungu ametujalia hivi vyanzo vya kutuingizia kipato kwenye Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa napenda kusisitiza kwamba sisi kama Bunge tuitake Serikali kuangalia upya mifumo ya usimamizi wa shughuli za Serikali ikiwemo watumishi wa umma. Watumishi wa umma hawawajibiki ipaswavyo. Tumelipa variations nyingi kwenye miradi ni kwa sababu tu kuna mtumishi mmoja au wawili hawakusaini GN mapema, basi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi ule wa Terminal Three, wakati tunaangalia Viwanja vya Ndege, tumemlipa BAM ile construction company ya Netherland faini ya Dola milioni 20 baada ya ku-negotiate. Walimtoza Dola milioni 50, ambayo ni sawa sawa na Shilingi bilioni 54 kwa sababu tu ya uzembe wa mtu mmoja au wawili walioko pale TRA na hazina kupitisha GN. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango mzuri. Ahsante sana.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania wa Mwaka 2022
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuomba kufanya marekebisho kidogo ya jina langu la kwanza ni Geoffrey na siyo Godfrey.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niendelee kuchangia Muswada huu wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania. Kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutusaidia tuweze kufika siku ya leo na tuweze kujadili Muswada huu kwa mustakabali wa nchi yetu. Kipekee nipende sana kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kuimarisha mifumo ya ufanikishaji uwekezaji kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka hivi karibuni Mheshimiwa Rais amefanya juhudi kubwa, kwanza alianza na slogan yake ya kufungua nchi, akimaanisha kwamba anawaalika watu wote wa ndani na nje ya nchi tuweze kushirikiana kujenga uchumi wa nchi yetu. Zaidi ya hapo Mheshimiwa Rais alifanya jambo kubwa la uzinduzi wa filamu ya Royal Tour na lengo kubwa lilikuwa ni kuitangaza nchi yetu akilenga maeneo ya uwekezaji pia kuimarisha shughuli za kuvutia utalii kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye michango yangu kuhusiana na Muswada huu wa Sheria ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, la kwanza kabisa, nchi yoyote duniani na sisi naamini kwamba ni pamoja na hao wengine, tunatakiwa tuguswe na masuala ya ajira kwa vijana. Kwa hiyo msingi wa kuwa na sheria au mabadiliko ya sheria kama haya au kuwa na sheria mpya kama hii pia ilenge kwenye kuhakikisha kwamba tunatengeneza fursa nyingi za ajira kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine tunatakiwa tupanue wigo wa kodi, Taifa lolote kuwa imara ni lazima liwe na uwezo wa kukusanya kodi ili kuhudumia bajeti yake. Kwa hiyo kitendo cha kuwa na sheria iliyo bora ya kuvutia, ya kuhamasisha uwekezaji na biashara, tafsiri yake tunatengeneza watu wengi wa kulipa kodi, iwe ni watu wa kiasili (natural persons) au iwe ni makampuni (legal persons). Kwa hiyo naamini kabisa sheria hii au Muswada huu umelenga kwenye kuibua fursa mpya au vyanzo vipya vya mapato kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sisi kama nchi tumesema wakati wote, kwamba tuna rasilimali nyingi kwenye nchi yetu, ni namna gani tunazitumia kwenye kubadilisha maisha ya wananchi wetu, naamini Muswada huu unalenga huko, lakini kijiografia tuko vizuri kama nchi ambayo tupo karibu na bandari kuu za kwenye eneo la Afrika Mashariki, pia tuna idadi kubwa ya watu. Mheshimiwa Rais jana ametutangazia kwamba tuna watu milioni 61, 741,120 kwenye nchi yetu, ni soko kubwa. Kwa hiyo ukijumlisha na soko la Afrika Mashariki na soko la SADC ni soko kubwa.

Mheshimiwa Spika, matarajio makubwa katika nchi yamewekwa kwenye sheria hii, kwa sababu unapokuwa na sheria mpya huwa mara nyingi inabeba matarajio ya watu. Watu wanajua kwamba kuna mambo mapya yanakuja kwa ajili ya kuimarisha mifumo iliyopo. Kingine tunakuwa na sheria mpya ili kuboresha ile sheria ya zamani, kuchukua mambo mapya ambayo tunafikiri ilikuwa ni changamoto katika utekelezaji wa ile sheria ya awali. Hali kadhalika sheria mpya hubeba hisia na ule usasa wa mawazo ya namna ya kuweza kuenenda kwenye eneo lile ambalo tutalikusudia na kwa case hii kwetu sisi ni eneo hili la uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, pia tunatakiwa tulenge kuboresha mifumo ya kitaasisi, kisera lakini hata kitaratibu zetu za utendaji wa kazi. Kwa hiyo tunaamini kwamba kulikuwa na ulazima wa Muswada huu wa sheria kuja Bungeni ili tuweze kuutendea haki na kuwapa nafasi wananchi wetu kuwa na mfumo bora wa kitaasisi pia kisera, mambo mapya ambayo tunayaingiza pia utaratibu wetu au working processes za kuhakikisha kwamba tunatoa huduma bora zaidi na kuepuka urasimu na vitu vingine ambavyo vimezungumzwa na wenzangu.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu pia Benki ya Dunia ilianzisha tangu mwaka 2008, walianzisha mpango wa upimaji taratibu za urahisi wa kufanya biashara kwenye nchi. Nchi ambazo zinapimwa ziko 190 kupitia moja ya group of companies za World Bank zinaitwa IFC (International Finance Corporation), tunapimwa ni namna gani taratibu zetu ni rahisi sana kwenye kufanikisha biashara. Kwenye hizi kuna viashiria 11 vimepangwa, kuanzia kwenye kuanzisha biashara mpaka kufunga biashara, hapo katikati kuna namna ya kupata mikopo, namna ya kuunganishiwa umeme, namna ya kulipa kodi, namna ya kupata vibali mbalimbali, kwa hiyo tunapimwa.

Mheshimiwa Spika, sasa Muswada huu naamini kwamba lengo lake kubwa pia ni kuhakikisha kwamba nchi yetu tunajipandisha kutoka nafasi ambazo tumezizowea 140,141, 190 tuje kwenye top 100 ili angalau tuweze kuheshimika duniani na kuaminika kwamba ni nchi ambayo tunavutia uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya nina ushauri, ukiangalia Muswada huu nia yake ni njema sana na niipongeze sana Serikali kwa sababu Muswada huu kwanza umechelewa kuja Bungeni. Nashukuru sana dhamira ya Serikali kutaka kuhakikisha kwamba tunajengewa mazingira sahihi zaidi ya uwekezaji ambapo tutatengeneza nafasi nyingine ya kutatua changamoto zote ambazo wenzangu wamezizungumza katika michango yao ya awali, lakini pia tuaminike kwa sekta binafsi kama wafanyabiasha ambao wao ndio tunawatarajia wawe ndio wazalishaji wakubwa wa fursa za ajira kwa vijana wetu. Serikali kawaida inaajiri watu mpaka 700,000 tu katika watu milioni 28 au 29 ambao wana uwezo wa kufanya kazi na wa zaidi ya miaka 18. Sasa hao wengine watakaoajiriwa na sekta binafsi, ni jukumu la Serikali na sisi kama Wabunge na Serikali kuona tunawasaidia kuweza kufungua hizo fursa ili vijana wetu wengi wapate ajira.

Mheshimiwa Spika, sasa nina mchango ufuatao kwenye baadhi ya maeneo. La kwanza, mawanda sasa sijui itakuwa ni Kiswahili sahihi au scope, coverage ya Muswada huu wa Sheria bado unafinya Sheria ya Uwekezaji hii ambao ndio inakuwa ni framework law, ni mother law, ni sheria kuu inaifinya isijihusishe na masuala yoyote ya uwekezaji kwenye madini, isijihusishe na wawekezaji kwenye petrol na gas wala kwenye kemikali hatarishi (hazardous chemicals) jambo ambalo nafikiri siyo sahihi kwa sasa. Naomba Serikali ifungue, sheria hii ndio sheria mama iweze kusimamia uwekezaji kwenye maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, tumekuwa tukizungumza kuhusu kutotabirika kwetu kwa vivutio ambavyo tunavitoa. Leo yametoka haya, kesho kuna maelekezo mengine yametoka, unakosekana mwelekeo. Napendekeza vivutio vyote ambavyo tunavifahamu standard, nchi za wenzetu wamefanya lakini sheria yetu yenyewe ya EPZA imetoa, tuviingize kwenye sheria badala ya kusubiri kukaa pembeni na kupata hisani ya mtu mmoja au kamati. (Makofi)

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, vilevile nilikuwa natamani sana niungane na …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia muda wako umeshaisha.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nilikuwa natamani niungane na wenzangu kwamba Kituo cha Uwekezaji sasa ifike wakati tukipe nguvu, kiwe ni commission kama wenzetu wanavyofanya kule Ethiopia, Egypt, Mauritius kule ni kituo chenye mamlaka, Uganda, Kenya ni Investment Authorities au Commission, kiwe na nguvu, kiwe na uwezo wa kuwa na a proper one stop center providing services kwa investors kuliko kuwa kama kilivyo sasa hivi kwamba ni kituo tu.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mwambe.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana basi naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Ulinzi wa Taarifa Binafsi wa Mwaka 2022
MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda kuomba kufanya marekebisho kidogo ya jina langu la kwanza ni Geoffrey na siyo Godfrey.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa niendelee kuchangia Muswada huu wa Sheria ya Uwekezaji Tanzania. Kwanza nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutusaidia tuweze kufika siku ya leo na tuweze kujadili Muswada huu kwa mustakabali wa nchi yetu. Kipekee nipende sana kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa dhamira yake ya dhati ya kutaka kuimarisha mifumo ya ufanikishaji uwekezaji kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka hivi karibuni Mheshimiwa Rais amefanya juhudi kubwa, kwanza alianza na slogan yake ya kufungua nchi, akimaanisha kwamba anawaalika watu wote wa ndani na nje ya nchi tuweze kushirikiana kujenga uchumi wa nchi yetu. Zaidi ya hapo Mheshimiwa Rais alifanya jambo kubwa la uzinduzi wa filamu ya Royal Tour na lengo kubwa lilikuwa ni kuitangaza nchi yetu akilenga maeneo ya uwekezaji pia kuimarisha shughuli za kuvutia utalii kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye michango yangu kuhusiana na Muswada huu wa Sheria ya Uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, la kwanza kabisa, nchi yoyote duniani na sisi naamini kwamba ni pamoja na hao wengine, tunatakiwa tuguswe na masuala ya ajira kwa vijana. Kwa hiyo msingi wa kuwa na sheria au mabadiliko ya sheria kama haya au kuwa na sheria mpya kama hii pia ilenge kwenye kuhakikisha kwamba tunatengeneza fursa nyingi za ajira kwa vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine tunatakiwa tupanue wigo wa kodi, Taifa lolote kuwa imara ni lazima liwe na uwezo wa kukusanya kodi ili kuhudumia bajeti yake. Kwa hiyo kitendo cha kuwa na sheria iliyo bora ya kuvutia, ya kuhamasisha uwekezaji na biashara, tafsiri yake tunatengeneza watu wengi wa kulipa kodi, iwe ni watu wa kiasili (natural persons) au iwe ni makampuni (legal persons). Kwa hiyo naamini kabisa sheria hii au Muswada huu umelenga kwenye kuibua fursa mpya au vyanzo vipya vya mapato kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sisi kama nchi tumesema wakati wote, kwamba tuna rasilimali nyingi kwenye nchi yetu, ni namna gani tunazitumia kwenye kubadilisha maisha ya wananchi wetu, naamini Muswada huu unalenga huko, lakini kijiografia tuko vizuri kama nchi ambayo tupo karibu na bandari kuu za kwenye eneo la Afrika Mashariki, pia tuna idadi kubwa ya watu. Mheshimiwa Rais jana ametutangazia kwamba tuna watu milioni 61, 741,120 kwenye nchi yetu, ni soko kubwa. Kwa hiyo ukijumlisha na soko la Afrika Mashariki na soko la SADC ni soko kubwa.

Mheshimiwa Spika, matarajio makubwa katika nchi yamewekwa kwenye sheria hii, kwa sababu unapokuwa na sheria mpya huwa mara nyingi inabeba matarajio ya watu. Watu wanajua kwamba kuna mambo mapya yanakuja kwa ajili ya kuimarisha mifumo iliyopo. Kingine tunakuwa na sheria mpya ili kuboresha ile sheria ya zamani, kuchukua mambo mapya ambayo tunafikiri ilikuwa ni changamoto katika utekelezaji wa ile sheria ya awali. Hali kadhalika sheria mpya hubeba hisia na ule usasa wa mawazo ya namna ya kuweza kuenenda kwenye eneo lile ambalo tutalikusudia na kwa case hii kwetu sisi ni eneo hili la uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, pia tunatakiwa tulenge kuboresha mifumo ya kitaasisi, kisera lakini hata kitaratibu zetu za utendaji wa kazi. Kwa hiyo tunaamini kwamba kulikuwa na ulazima wa Muswada huu wa sheria kuja Bungeni ili tuweze kuutendea haki na kuwapa nafasi wananchi wetu kuwa na mfumo bora wa kitaasisi pia kisera, mambo mapya ambayo tunayaingiza pia utaratibu wetu au working processes za kuhakikisha kwamba tunatoa huduma bora zaidi na kuepuka urasimu na vitu vingine ambavyo vimezungumzwa na wenzangu.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu pia Benki ya Dunia ilianzisha tangu mwaka 2008, walianzisha mpango wa upimaji taratibu za urahisi wa kufanya biashara kwenye nchi. Nchi ambazo zinapimwa ziko 190 kupitia moja ya group of companies za World Bank zinaitwa IFC (International Finance Corporation), tunapimwa ni namna gani taratibu zetu ni rahisi sana kwenye kufanikisha biashara. Kwenye hizi kuna viashiria 11 vimepangwa, kuanzia kwenye kuanzisha biashara mpaka kufunga biashara, hapo katikati kuna namna ya kupata mikopo, namna ya kuunganishiwa umeme, namna ya kulipa kodi, namna ya kupata vibali mbalimbali, kwa hiyo tunapimwa.

Mheshimiwa Spika, sasa Muswada huu naamini kwamba lengo lake kubwa pia ni kuhakikisha kwamba nchi yetu tunajipandisha kutoka nafasi ambazo tumezizowea 140,141, 190 tuje kwenye top 100 ili angalau tuweze kuheshimika duniani na kuaminika kwamba ni nchi ambayo tunavutia uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema haya nina ushauri, ukiangalia Muswada huu nia yake ni njema sana na niipongeze sana Serikali kwa sababu Muswada huu kwanza umechelewa kuja Bungeni. Nashukuru sana dhamira ya Serikali kutaka kuhakikisha kwamba tunajengewa mazingira sahihi zaidi ya uwekezaji ambapo tutatengeneza nafasi nyingine ya kutatua changamoto zote ambazo wenzangu wamezizungumza katika michango yao ya awali, lakini pia tuaminike kwa sekta binafsi kama wafanyabiasha ambao wao ndio tunawatarajia wawe ndio wazalishaji wakubwa wa fursa za ajira kwa vijana wetu. Serikali kawaida inaajiri watu mpaka 700,000 tu katika watu milioni 28 au 29 ambao wana uwezo wa kufanya kazi na wa zaidi ya miaka 18. Sasa hao wengine watakaoajiriwa na sekta binafsi, ni jukumu la Serikali na sisi kama Wabunge na Serikali kuona tunawasaidia kuweza kufungua hizo fursa ili vijana wetu wengi wapate ajira.

Mheshimiwa Spika, sasa nina mchango ufuatao kwenye baadhi ya maeneo. La kwanza, mawanda sasa sijui itakuwa ni Kiswahili sahihi au scope, coverage ya Muswada huu wa Sheria bado unafinya Sheria ya Uwekezaji hii ambao ndio inakuwa ni framework law, ni mother law, ni sheria kuu inaifinya isijihusishe na masuala yoyote ya uwekezaji kwenye madini, isijihusishe na wawekezaji kwenye petrol na gas wala kwenye kemikali hatarishi (hazardous chemicals) jambo ambalo nafikiri siyo sahihi kwa sasa. Naomba Serikali ifungue, sheria hii ndio sheria mama iweze kusimamia uwekezaji kwenye maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili, tumekuwa tukizungumza kuhusu kutotabirika kwetu kwa vivutio ambavyo tunavitoa. Leo yametoka haya, kesho kuna maelekezo mengine yametoka, unakosekana mwelekeo. Napendekeza vivutio vyote ambavyo tunavifahamu standard, nchi za wenzetu wamefanya lakini sheria yetu yenyewe ya EPZA imetoa, tuviingize kwenye sheria badala ya kusubiri kukaa pembeni na kupata hisani ya mtu mmoja au kamati. (Makofi)

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, vilevile nilikuwa natamani sana niungane na …

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja malizia muda wako umeshaisha.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Nilikuwa natamani niungane na wenzangu kwamba Kituo cha Uwekezaji sasa ifike wakati tukipe nguvu, kiwe ni commission kama wenzetu wanavyofanya kule Ethiopia, Egypt, Mauritius kule ni kituo chenye mamlaka, Uganda, Kenya ni Investment Authorities au Commission, kiwe na nguvu, kiwe na uwezo wa kuwa na a proper one stop center providing services kwa investors kuliko kuwa kama kilivyo sasa hivi kwamba ni kituo tu.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Mwambe.

MHE. GEOFFREY I. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana basi naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)