Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Tumaini Bryceson Magessa (33 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, namshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipa nafasi ya kuweza kuongea mbele ya Bunge hili. Nawashukuru sana wananchi wa Jimbo la Busanda kupitia Chama Cha Mapinduzi walionipatia kura za kutosha na leo nawawakilisha kama Mbunge ndani ya Bunge hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia ya Bunge la Kumi na Moja, lakini katikati kulikuwa na achievement speech, ilikuwa katikati tarehe 16 Juni, kulikuwa na taarifa tena ndani ya Bunge hili ambayo Rais alionesha mambo yaliyofanyika. Mwezi Novemba tumekuwa na hotuba nyingine ambayo tunaizungumzia leo Bunge la Kumi na Mbili, Bunge letu la kwanza la Kumi na Moja lilionesha dira na falsafa ya Mheshimiwa Rais anakotaka kuipeleka nchi hii, lakini tarehe 16 Juni, alionesha yale yaliyofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi wote ni mashahidi nikiwemo mimi kwenye taarifa hizi na kwa macho yetu, hakuna sekta aliyoizungumzia ambayo haikufanyiwa maboresho. Kama ni barabara, kiwango cha cha lami kimeongezeka, lakini kama ni barabara za TARURA zimeongeza, japokuwa zinaharibika kila mvua inaponyesha. Vituo vya afya vimeongezeka vimejengwa vipya 1,769, katika hivyo zikiwepo hospitali za mkoa, ikiwemo vituo vya afya. Hii inaonesha wazi kwamba dira na falsafa iliyokuwa imetolewa imetekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye hotuba hii ya Bunge la Kumi na Mbili ambapo ndipo kuna kazi kubwa tunatakiwa kufanya sisi, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, yapo maono makubwa ambayo nimeyaona kwenye hotuba hiyo na wataalam kazi kubwa tuliyonayo sasa sisi kama Wabunge hasa nikiwemo mimi ni kwenda kuhamasisha yale yaliyoandikwa huko ndani yaweze kutokea. Kwa sababu hotuba ni kitu kimoja lakini utekelezaji ni kitu cha pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika sekta ya afya page namba 65 wameonyesha wazi kwamba sasa tunakwenda kwenye bima kwa wote. Mtego upo kwa Waziri wa Afya, tunapokwenda kwenye bima kwa wote kipi kilianza kati ya kuku na yai, ni kuku au yai? Inaanza kwanza huduma iwe bora ili watu wahamasike kuingia kwenye Bima ya Afya au bima ya afya kwanza ndiyo huduma iwe bora? Kwa hiyo, kuna kazi fulani wataalam wanatakiwa kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tumesema kwenye ukurasa namba 44, STAMICO itaboreshwa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wachimbaji wadogo wa madini wanasaidiwa. Kazi kubwa tuliyonayo ambayo naiona Rais ametuwekea mezani hapa, je, huduma hizi tunazotaka kuzifanya wataalam tulionao na sisi wenyewe tunazo service level agreement zetu? Kwa sababu inaonekana mwananchi anaweza kuwa huduma katika level yoyote, service level agreement ni ipi, kiwango gani cha huduma tunatakiwa tumpe, hapo ndiyo kuna changamoto. Tunaye Afisa Kilimo je, anakwenda kwenye shamba darasa na haya mashamba tunayoyazungumza hapa ndani ambayo yanaonekana yatakuwa ni mikataba kati ya wanunuaji na wakulima wenyewe yapo, anaweza kuwa haendi kule.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunatakiwa service level agreement na watu wetu nini wa delivery. Kwa sababu unamuuliza mtu anakwambia nimeingia kwenye OPRAS, nimeingia sijui wapi, anaonekana anafanya vizuri lakini ukimuuliza kuna shamba darasa mahali hakuna. Kwa hiyo, mimi najielekeza kama Mbunge kuingia kwenye maeneo haya kuona namna gani tutafanya ili viongozi sisi pamoja na wataalamu wetu waweze kutoa kile ambacho Mheshimiwa Rais anatarajia hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo mengi yaliyozungumzwa hapa ambayo nategemea yakifanyika tutakapokwenda kufunga Bunge hili tutakuta maendeleo yetu yamekwenda kasi. Ninao mfano mmoja mdogo, nilipokuwa natoka kwenye kampeni nafika airport Dar es Salaam nilimwambia mtu mmoja usinipitishe Ubungo kwa sababu tukipita huko wanajenga ile interchange itatuletea shida. Akaniambia wewe inaonekana ni wazamani sana kumbe barabara ilishakamilika, tukapita pale juu na bahati mbaya alikuwa ni mwanangu ananiambia baba wewe umepitwa na wakati, tukapita juu tukashuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, yapo mambo makubwa yamekwishafanyika, tutowe nafasi sasa na akili zetu kuhakikisha kwamba yale yaliyosemwa yanaweza kutokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nisitumie muda mrefu sana, naomba niunge mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, mradi wa maji kutoka Nungwe kwenda Mgodini GGM unatoa maji ghafi katika kata ya Nyamwilolelwa hususani Kijiji cha Kayenze, naiomba Wizara iyatibbu maji haya kabla ya kutumiwa na wananchi. Please establish a treatment plant before human consumption.

Mheshimiwa Spika, mradi unaoendelea wa kuleta maji katika miji midogo ya Katoro na Buselesele toka chanzo cha Chankorongo uongezewe kasi ya utekelezaji, lakini kutokana na ukuaji wa kasi wa miji hii Wizara iongeze pesa katika kupanua mtandao wa maji kila mwaka katika maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Busanda linayo miradi ya visima vya maji iliyo kwenye utekelezaji, niombe itakapokamilika tupate pesa ya mtandao wa maji kwenye vijiji husika.

Mheshimiwa Spika, nawapongeza RM na DM kwa ushirikiano wao kuhakikisha Jimbo la Busanda wananchi wanakunywa maji safi na salama.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, ubora wa vituo vya afya vya Chikobe na Bukoli Jimboni Busanda vinahitaji Wizara ya Afya isimamie huduma (qualify of service) na uboreshaji wa miundombinu ili wananchi wahudumiwe vyema.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia fursa hii, lakini namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipatia nafasi hii ya kuchangia leo hotuba ya bajeti ya mwaka 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa uendelevu wa kukusanya mapato ya ndani ambayo ni chanya. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa usimamizi mzuri, na Mawaziri wengine wa kisekta. Kumbukumbu zinanionesha hapa mapato yetu ya ndani, ukurasa namba saba, mwaka 2020/2021 yalikuwa trilioni 20.59, lakini 2021/2022 tukapata trilioni 24.4, hii 2023 ambayo ndiyo tunayo sasa mpaka Aprili tulikuwa na trilioni 21.67.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapato yetu ya kutoka TRA kwa mwezi sasa yamepanda kuwa trilioni 2.63. kwa hiyo ukiangalia miezi iliyobaki hapa yatavuka trilioni 24 ya mwaka jana; ndiyo sababu nikasema kuna ongezeko chanya. Kwa hiyo nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuhakikisha kwamba hili limesimamiwa na mapato yetu hayaendi kushuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hili vilevile niwapongeze wale waliweza ku-introduce teknolojia hapa. Kuna EFD inafanya kazi kubwa ya kutoa risiti kwenye maeneo yetu. Kwa bahati mbaya sana watu wengi hawana uzoevu wa kuomba risiti na mwisho wa wakati ni kwamba kuna mahali mapato ya Serikali yanapotea. Kwa hiyo kwa hili pamoja na kushauriana sisi wenyewe lakini tunashauri vilevile wafanyabiashara wote wajiandae kuhakikisha kwamba wanapouza watoe risiti na sisi tunapoenda kununua tuombe risiti kwa ajili ya kuhakikisha mapato ya Serikali yanaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ETS ambayo nayo imesaidia kwamba bidhaa zetu zimekuwa stamped tuongeze tu wigo wa hiyo stamping kuhakikisha kwamba sasa tunaweza kuzitambua na mapato yetu yanaweza kuendelea kuongezeka yavuke hiki ambacho tunakiona. Maana tukiendelea kuwa na mapato mengi ya ndani kuna wakati tutafikia kama tukifanya vizuri sana tunaweza ku-support bajeti yetu kwa asilimia hata 75. Tukienda huko maana yake ni kwamba sasa tutakuwa tumeanza kusogea mbele zaidi kuliko ambako sasa hivi tuko. Kwa hiyo ushauri wangu kwenye Serikali hapa tuendelee kuangalia vyanzo vingine kuhakikisha kwamba mapato ya ndani yanaongezeka yaweze ku-support bajeti na miradi yetu mingi iwe financed kutoka kwenye mapato yetu wenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili nitakalochangia ni sekta za uzalishaji, mara nyingi hupenda kuzizungumzia sana. Ili uchumi wetu uchangamke hatuna majibu rahisi, ni lazima sekta za uzalishaji zizalishe sana na mchango wa Pato la Taifa kutoka kwenye kilimo, mifugo na hata uvuvi uwe mkubwa. Ukishakuwa mkubwa, maana yake uchumi wetu utachangamka. Kwa nini nasema utachangamka? Mnajua kabisa dhima yetu ni kuwa na uchumi shindani na shirikishi. Sasa ili uwe shindani na shirikishi lazima tuwashirikishe wananchi wengi zaidi; na hawa wengi wameajiriwa kwenye kilimo, uvuvi na mifugo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia hapa kwenye ukurasa namba 11 mwaka 2021/2022 tulibajeti kilimo bilioni 294 lakini mwaka 2022/2023 tukabajeti 954.0 billion. Mwaka huu tuna billioni 970.8 kuna ongezeko la kama bilioni 16.8 hivi. Hii nikiangalia mimi naiona kama ni ndogo kwa sababu ya ushirikishi ule wa wananchi wengi. Ningeomba tu twende tuangalie kwenye Malabo Declaration itakayotupeleka kwenye 10 percent kadiri tunavyozidi Kwenda, ili tuendelee kuhakikisha kwamba kilimo sasa kinaweza kuwa ndio uti wa mgongo wa Taifa. Kwa sababu tulitangaza kilimo uti wa mgongo wa Taifa kikiwa kinapewa bajeti ya bilioni 200. Sasa uti wa mgongo unaopewa bilioni 200 nafikiri maneno yalikuwa yamekosewa. Kwa hiyo niwaombe sana niishauri Serikali tuendelee kuongeza pesa eneo hili ili watu wengi waendelee kuajiriwa na kushirikishwa katika uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaweza tukaona kwa bajeti ile ya mwaka jana imesaidia upatikanaji wa pembejeo za kilimo lakini imetupatia kilimo cha mashamba makubwa (broke farms) ambayo yameanza sasa kuratibiwa na Waziri muhusika. Vilevile imepewa ruzuku ya mbolea kwa wakulima, imeanza kushughulika na ujenzi wa skimu za umwagiliaji, na mwisho inatakiwa iendelee kuimarisha upatikanaji wa masoko ya mazao ya kilimo. Ukiyaona haya yote yaliyotajwa kama yametekelezwa na yakitekelezwa vizuri maana yake hapa ndipo palipo na majibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kulima sana ni lazima uchumi wetu uwe unaongozwa na soko, kwamba demand ya hiki kitu iko wapi, mahindi yanatakiwa wapi, alizeti inatakiwa wapi. Kama inatakiwa kwa wingi na hicho ambacho kinaonekana kwamba bei yake ikawa nzuri zaidi wakulima wataendelea kulima kwa nguvu zote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais ametoa ruzuku, lakini mwaka jana nilishauri Serikali kwamba ruzuku ile ya mbolea iliyotolewa wakulima wengi hawakufaidika nayo kwa sababu vituo vya upatikanaji wa mbolea vilikuwa mbali na wananchi. Mwaka huu viongezwe ili kuhakikisha kwamba vinawakaribia wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ruzuku hii wananchi wengi ambao walitakiwa kujiandikisha hawakujiandikisha wengine. Kwa hiyo tuombe sana sasa daftari la kujiandikisha lifanyiwe uhariri upya ili wajiandikishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine hii ruzuku ya mbolea iliyotolewa hapa tuhakikishe kwamba huduma za ugani kutoka kwa hawa maafisa ugani zinapatikana ili wananchi wajue ni namna gani ya hiyo ruzuku ya mbolea kuitumia kwa ajili ya uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa kwenye kilimo hapa nizungumzie skimu za umwagiliaji. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwamba niliona hata kule Buzanda kuna skimu sasa hata ya kutengeneza kutoka Ziwa Victoria. Najua na maeneo mengine yanayozunguka Ziwa Victoria yanatengeneza skimu. Kwenye hili upembuzi yakinifu ufanyike mapema kwenye maeneo yetu ili skimu hiyo zianze kufanya kazi; badala ya wananchi kuzalisha mara moja wazalishe mara tatu na uchumi wao utakuwa umepanda, na uchumi ukipanda tutakuwa tayari tumepata uchumi shindani na shirikishi na hivyo uchumi wetu utaonekana sasa ni shindani hapa duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya hifadhi ya chakula. Nimeziona tani 400,000 zinatakiwa kuhifadhiwa, sina uhakika kama maeneo mengine walipata shida kama ya kwangu kwamba debe la mahindi mwaka jana lilifikia shilingi 25,000 mpaka 27,000. Kwa hiyo niombe sana uhifadhi wa chakula ufanyiwe kazi kwa umakini zaidi ili inapotekea crisis kama iliyotokea mwaka jana au mwaka huu wa fedha Serikali iwe na uwezo wa kuwasaidia wananchi wasikutane na bei ambazo sasa hawawezi kununua tena. Ninaamini hili likifanyika mambo yatakuwa mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna sekta nyingine ya uzalishaji ambayo ni ya uvuvi. Nimeona wanasema watanunua boti 160 wameshanunua 118. Kuna kitu cha kufanya hapa. Kwenye uvuvi ndani ya nchi hii jirani yangu tu Mwijage hapa boti 160 zikipelekwa hazitoshi, nchi nzima boti 160? Hapa naomba tu Mheshimiwa Waziri wa Fedha hebu waangalieni kwa jicho la huruma hawa watu wa uvuvi. Hatuwezi kupeleka boti 160 nchi nzima tukasema tumeenda kuchangamsha sekta ya uvuvi, tutakuwa bado hatujafanya kitu cha maana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye mifugo ukiangalia bado tuna hoja kubwa ya malisho. Kwa hiyo mifugo tuliyonayo haina tija, tuna mifugo mingi lakini ukiangalia ng’ombe mmoja anatoa lita moja, bado hakuna tija kwenye sekta hii. Kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha hili liangaliwe upya kuona namna gani tunaweza kutengeneza sekta yetu hii hizi za uzalishaji zikaweza kuwa na tija na uchumi wa nchi ukaweza shindani na shirikishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba hii kitu cha tatu nilitaka kuchangia niwapongeze sana Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri. Kulikuwa na hoja ya vijana wanaosoma kwenye vyuo vyetu vya DIT, Mbeya University na Arusha Technical Collage. Hawa wanamaliza form four wanakwenda kule kimsingi ni kama wale wanamaliza form four kwenda form five na form six, lakini wao walitakiwa walipie ada. Sasa hii ada hawa ni watoto wa wakulima lakini Serikali kupitia Mheshimiwa Rais, Rais makini Dkt. Samia Suluhu Hassan ameliona hili kwamba sasa hawa watu wa DIT wameondolewa ada hiyo. Hizi tertiary institutes tunazihitaji sana kwa ajili kutengeneza kupata mafundi wa viwanda vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri mimi huko nyuma nilisoma nikiwa tech…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Tumaini Magessa.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, rejea kiambatanisho cha miradi (minara itakayojengwa mwaka 2022/2023) kwenye hotuba (soft copy) iliyo katika Wilaya ya Geita Jimboni Busanda inaonesha Bujila na Nyamalimbe ambayo ni ya mwaka uliopita 2021/2022, kitabu cha hotuba kinaonesha kiambatanisho sahihi ambapo inaonesha ujenzi utafanyika Nyakagomba (Kata ya Nyakagomba) na Msasa (Kata ya Busanda) mwaka 2022/2023. Naomba kiambatanisho kwenye softcopy ya hotuba irekebishwe ifanane na printed hard copy.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, lakini namshukuru sana Mwenyezi Mungu vilevile kutupa nafasi ya kuweza kujadili hotuba hii ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii nilikuwa napitia randama, nikaona wazi kwamba katika malengo makubwa ya Wizara ya Nishati moja ni kuongeza uzalishaji, kuboresha mfumo wa usafirishaji na usambazaji wa umeme. Sasa nikawa najaribu kuangalia Waziri anapozungumza ni mahali gani anagusa kuongeza uzalishaji na ni wapi ripoti hii inaongeza kama anaongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu nifanye marekebisho kwamba katika kuongeza uzalishaji inawezekana hii leaflet haikuonesha Bwawa la Nyerere, lakini kwenye vipaumbele vya Wizara hii kwenye randama kipengele “A” kinaonesha Bwawa la Julius Nyerere kwa hiyo inawezekana katika usomaji kuna mahali watu wamesoma tu haraka haraka lakini imeonyeshwa ndio namba moja kwenye vile vipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na timu yako nzima ambayo wachangiaji wameonesha namna ulivyo na wataalam wazuri, lakini Mheshimiwa Waziri niseme tu wazi mimi ningeulizwa leo mahali gani kuna shida kule kwa wananchi wetu pamoja na uzalishaji huu unaosemwa, ningezungumza shida tunayoipata kubwa ni kutokana na wananchi wetu kuwa na ahadi ya vijiji kadhaa kumaliziwa kupewa umeme na havijapewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa na jirani yako anakula, halafu wewe unalala njaa pembeni, unaweza ukajua malalamiko uliyonayo ndani ya moyo na hata ndani ya kusema, kwa hiyo kuna watu wengi ambao tunao kule kwenye vijiji vyetu wanalalamika kwa sababu umeme haujafika kwao. Lakini nikupongeze kwa sababu kama nilivyosema malengo haya ambayo nimesema umeonesha wazi kwamba kuna uzalishaji unakwenda kufanyika sasa shida ambayo naiona katika vile vipaumbele kuna vipaumbele kutoka “A” mpaka “U”; sasa “A” mpaka “U” vinanionesha kama ni vingi sana na hii pesa ambayo niseme tu kwenye randama inasomeka bado ni shilingi trilioni 2.7 lakini hapa imesemwa shilingi trilioni 2.9 maana yake kuna mahali fulani hapajarekebishwa hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nisema pesa hii nina mashaka sana kwenye utekelezaji kama inaweza kufanya haya mambo ambayo yameandikwa huku, kwa hiyo inawezekana mipango ikawa mizuri sana, lakini mwisho wa siku tutakapoanza kuteleza tukaingia kwenye mahali fulani ambako tunashindwa kuitekeleza. Kwa hiyo, niombe sana nikiona hapa kama nilivyosema “A” mpaka “U” inaonesha tuna sehemu tunakwenda kuongeza umeme uzalishaji JK Nyerere megawati 2115.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna Ruhuji megawati 358; Lumakari megawati 222; Kinyerezi megawati 185; Lusumo megawati 80; Malagalasi megawati 47.5; ukiangalia Somanga kuna megawati 330 na sehemu zingine nyingi ambazo zinaonekana kwamba lengo letu inaonekana ni kubwa na mpango wetu mkubwa kwenye hotuba hii ni kufikia megawati 5,000 ifikapo mwaka 2025/2026. Sasa nikawa na mashaka hapo kwamba je, hii allocation ya fedha ambayo tunaisema hapa, itatupeleka kutengeneza na tufikishe megawati 5000 kama tulivyoandika hapa maana tusife mahali tukawa na mipango mizuri kubwa resources zetu hazitoshi.

Kwa hiyo, niombe sana kwenye hoja hii tuhakikishe resource tunazozizungumzia tuna mahali tunaweza kwenda kuzipata ili tuzipate megawati 5000 kwa sababu wananchi wanahitaji umeme sasa, mwanzo umeme ulikuwa ni hanasa lakini sasa hivi kila mmoja ana uhitaji kwa ajili ya shughuli za maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna usafirishaji nimeona hapa kuna Rufiji Chalinze - Dodoma Kv 400; kuna Chalinze - Kinyerezi Kv 400; Singida – Arusha - Namanga Kv 220; kuna Rusumo - Nyakanazi Kv 220; kuna Geita - Nyakanazi Kv 220. Sasa nisimame hapa kwenye Geita - Nyakanazi hapa, ndipo Jimbo la Busanda vijiji kadhaa vinategemea vipate umeme kwenye mradi huu wa Geita - Nyakanazi. Hapa vimeandikwa kwamba kuna allocation ya shilingi bilioni 6.53; mradi huu umekuwepo muda mrefu, unajengwa na hauishi, kwa hiyo mahali fulani kwenye vijiji ambayo tunategemea vipate umeme kutoka kwenye mradi huu imeendelea kuwa ni mazungumzo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwanzo nilisema ni nguzo za umeme, lakini baadaye imezungumzwa kwamba sasa kama hapa inatakiwa kwenda kumaliziwa, sina uhakika kama mradi huu utamaliziwa kwa wakati ili wananchi waweze kupata umeme kutoka mradi huu wa Geita – Nyakanazi; kuna Bulyanhulu - Geita Kv 220; kuna North-West Grid Extension ambayo inaenda Mbeya, Sumbawanga, Mpanda, Kigoma na Nyakanazi iko mingi ambayo imeandikwa hapa, lakini more interesting ni mradi ule ambao mnakwenda kuhakikisha kwamba sasa mnaenda ku-rectify SGR.

Mheshimiwa Mwenyekiti, umeme kwenda kwenye SGR ambayo sasa hivi ipo kwenye construction, tunategemea kabisa hapa pawe muhimu sana kwa sababu bila umeme maana yake hatutaweza ku-oparate. Sasa inaonekana katika miradi hii ambayo imeandikwa hapa, hiyo SGR rectification ni sehemu yake. Kwa hiyo, niwaombe sana tuhakikishe kwamba tunakwenda kufanya hivi vitu ili wananchi wetu waweze kuona maendeleo ambayo tumekwisha waambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna kipengele “C” ambacho ni cha kuendeleza miradi ya nishati vijijini kupitia Wakala wa Nishati Vijijini, hapa kuna changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimboni Busanda mwaka jana kwenye hotuba hii kwenye bajeti hii tulionesha kuna vijiji 57 havina umeme, REA wakaonekana tumepata mkandarasi, mkandarasi yule akaonekana baadaye alikuwa anaonekana performance bond hana, tumepata mwingine, lakini mpaka leo ninavyozungumza mwaka jana vilikuwa 57 na mwaka huu ni 57. Sasa kama tunapima KPI tunataka kuona utekelezaji umefanyikaje mwaka jana vilikuwa 57 na mwaka huu bado viko 57, niwaombe sana unaweza ukajua ilivyo vigumu kusimama kwenye mkutano wa wananchi ukawaeleza mwaka jana vijiji 57 vilikuwa havina umeme, halafu wanakuambia vingapi umeshaweka umeme mwaka huu unasema bado viko 57, kwa hiyo wewe una nafanya zero performance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuombe sitaki kusema Waziri una zero performance kwenye hili, lakini Mbunge ndiye ana zero performance kwa sababu wananchi wanajua hajafanya kitu chochote. Sasa niwaombe sana kwenye REA hapa kwamba kama tumewaambiwa wananchi kuna vijiji 3,617 basi kazi ianze kuonekana, tuanze kuonekana kama vijiji vinapungua ili kufika mwaka 2025 kuwe na mahali fulani wananchi ambao walikuwa hawana umeme wameshapata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi juzi nimepewa t-shirt kwenye semina ya hapa t-shirt imeandikwa nyuma sasa tunaingia vitongoji vyote, huku nyuma ya t-shirt yangu nimeogopa kuivaa kwa sababu wananchi wanaweza wakanipiga mawe, kwamba mimi jimbo langu lina vijiji 84, halafu nina vijiji 26 tu vyenye umeme na vijiji 58 havina umeme, halafu nitembee na tisheti nyuma imeandikikwa kwa sababu tunaingia kwenye vitongoji wataniuliza, are you mad? Umekuwaje tena? Yaani mmeingia kwenye vitongoji wakati vijiji havina umeme, mbona mmeruka? (KIcheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana nataka hii t-shirt niivae, lakini naomba sasa nihakikishiwe kwamba nikiivaa tunapata kweli umeme kwenye vijiji na baadaye twende kwenye vitongoji? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna sehemu “D” kwenye randama kuanzisha maandalizi ya kupeleka umeme katika vitongoji vyote ambayo iko ukurasa wa saba kwenye randama yetu, niwapongeze sana kwa hili kama kuna mahali wananchi wanapata shida ni ile kilometa moja tulio-supply umeme yaani mtu umemuonjesha biriani, lakini biriani yenyewe ilikuwa ni punje 10 sasa anatamani aanze kula biriani imekwisha, hebu tuwapelekee nimefurahi sana kusikia sasa unatuongezea kilometa mbili, sijui zinaanza lini hizi, ili walau hizi kilometa mbili hizo zionyeshe kwamba kuna mahali sasa wananchi wameongezewa hii peripheral ya kilometa moja ilikuwa inatuletea ukipiga zile nguzo span ya mita 50 ni nguzo 20; lakini ukipiga span ya mita 100 maana yake ni habari ya nguzo kumi na ngapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana ili wananchi wetu waweze kuona maandalizi haya tunayafanya kwenye vitongoji na nyongeza tulioifanya, lakini wako wananchi wengi wameamasika kuweka umeme kwenye nyumba zao na bahati mbaya hapa katikati tumeambiwa mita hakuna, kwa hiyo wananchi wengi wamekwisha fanya wiring, wamekwisha fanyiwa survey, lakini umeme hauendi kwao kwa sababu mita hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa niliyokuwa nayo mchana wa leo ni kwamba mita kadhaa zimeenda, lakini kuanzia wale waliofanya wiring na kuwa surveyed kuanzia mwezi wa pili kuja mwezi wa tano hapa bado mita zile hazitoshi. Niombe sana wananchi wale wapate umeme, maeneo mengi sitaki kuyataja hapa wako wananchi kila anayekupigia simu anaonesha amemaliza hii kazi wiring, amekuwa surveyed lakini hawezi kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi niwaombe sana wataalam Mheshimiwa Waziri kwa sababu scope ya kazi wanaijua, kama scope ya kazi wanaijua maana yake wanajua ni mita ngapi zinahitajika, ni nguzo ngapi za LV zinahitajika, ni wire kiasi gani za copper au aluminum zinahitajika, insulator kiasi gani zinahitajika kuunganisha huu umeme. (Makofi)

Sasa ni mahali gani ambako tunafika mahali tanafanya mradi utekelezeke, lakini tunavyoenda kutekeleza mita 800 hamna, mita 10000 hakuna, hii inakujaje? Kwa hiyo niombe sana tunapokwenda kwenye mradi ambao tayari tutakaa mezani kuandika kwenye makaratasi, scope ya kazi inajulikana, tutatengeneza chart activities zetu tufike mahali kwamba tuna vijua vile vitu tuviagize vije ili wananchi wetu wasifike mahali ameshalipa amefanya wiring lakini anaonekana umeme anasubiri mita.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna watu toka mwaka jana mwezi wa 10 walikuwa hawajafungiwa umeme, leo ni mwezi wa tano miezi saba na ameshalipa pesa yake hii pesa angelipia mwanafunzi ada, sasa kwa nini aliingiza huku lazima naye ana vipaumbele vya alifikiri angepata umeme azalishe, halafu alipie mwanafunzi ada, sasa imekaa miezi saba, mtoto hajaenda shule, kwa hiyo, niwaombe sana kwa sababu scope tunayo tuwe tunafanya makadirio ambayo yanaweza yakafanya wananchi wetu waweze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Jimboni Busanda kila siku nimekuwa ninasema sisi ni wachimbaji wa dhahabu, sisi ni wakulima, nilitegemea sana umeme uje kule ili hizo maximum demand hizo KVA tuweze kuwalipa, sasa nashangaa inaonekana umeme unaenda mahali kwenda tu kwenye matumizi ambayo ni domestic wakati matumizi ya viwanda yalitakiwa yazalishiwe kule Busanda umeme haufiki. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri inawezekana jicho lako lilikuwa halijachungulia Busanda kwa ukubwa wake nikuombe sana ulete tuchimbe dhahabu kwa kutumia umeme huu ambao tunausema leo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kunipatia nafasi ya kuongea katika Bunge hili kuchangia katika Mpango huu wa Maendeleo wa Miaka Mitano na wa Mwaka Mmoja. Ni dhahiri kwamba, ukurasa wa tano umeonesha wazi kwamba, nguzo za Mpango huu wa Maendeleo zimejikita kwenye sehemu tatu; ya kwanza ni utawala bora. Utawala bora sina mashaka kwa namna ambavyo unaendeshwa sasa kwa sababu ya haki na uwajibikaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nguzo ya pili ni ukuaji wa uchumi; ukuaji wa uchumi tumeuona kwamba, uchumi unakua, lakini kuna mambo kadhaa ambayo tunatakiwa tuyapitie. Wabunge wengi wameeleza juu ya kilimo, ni kweli kabisa kwamba, Watanzania zaidi ya asilimia 75 wameajiriwa kwenye kilimo na bajeti tunayoipeleka kwenye kilimo ni ndogo sana. Kama hiyo graph ya ukuaji wa uchumi ni linear maana yake tunapoondoa tu kuwafanya wale wasihusike katika uchangiaji wa pato la Taifa, lazima uchumi wetu utaonekana haukui haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo iko hoja tunataka kuongeza bajeti, lakini sisi tunaotoka vijijini kule watu wamezalisha mchele haujauzwa hadi leo upo, mahindi yapo yamezalishwa hayajauzwa. Maana yake kuna hoja ya masoko hapa haijakaa vizuri ndani ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ndugu zangu wanaitwa TMX, wameshughulika na suala hili, lakini kila mmoja ana mpunga ndani, ana mahindi ndani na biashara haifanyiki. Kwa hiyo, tunapokwenda kwenye hoja hii, lazima tutafiti tujue kwamba, tuna masoko ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tuna udongo wa kila aina mahali tunapoishi. Hii Wizara ya Kilimo inatakiwa ipewe fedha kwa ajili ya utafiti. Kuna mahali fulani niliwahi kuishi wakaniambia hapa hapahitaji mbolea udongo wake una madini mengi sana, maana yake hawana elimu ya kutosha kujua nini wanatakiwa kufanya kwenye kuzalisha. Kwa hiyo, niseme tu wazi tunahitaji kuchangia kwa kiwango kikubwa kwenye Wizara ya Kilimo, ili tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye ukuaji wa uchumi, ukiangalia vipaumbele kwenye ukurasa wa 101 inasema wazi kwamba, tutachochea uchumi shirikishi na shindani, lakini ukirudi kwenye ukurasa namba 64 kwenye Mpango huu, utagundua kwamba, kuna mahali fulani sekta binafsi haikuhusika vizuri kuna vitu ambavyo vilikwenda vya kichefuchefu. Ukiangalia Clause 3(iii), utagundua kuna habari ya ulipaji wa kodi imeandikwa pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ninakotoka Katoro nina wafanyabiashara zaidi ya 5,000 pale Mjini Katoro, wana ugomvi na TRA kuanzia asubuhi hadi jioni. Nina mashaka sasa kama tunataka kukuza uwekezaji na uchumi, hiyo ni katika kipaumbele cha tatu, inaonekana kuna tatizo kati ya TRA na wafanyabiashara, tutakuzaje sasa uwekezaji na uchumi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima sasa hivi tuanze kutengeneza kama ni ushirikishi na shindani tuhakikishe kwamba, TRA wanafanya urafiki na hawa wafanyabiashara wasiwakadirie vitu ambavyo havipo. TRA wamekuwa wanarudi nyuma miaka mitano halafu wanamwambia mtu sasa unatakiwa kulipa milioni 300; milioni 300 na yeye mtaji wake ni milioni 150, kimsingi huyu amefilisika. Kwa hiyo, niombe sana hoja yetu ya msingi ni kuhakikisha kwamba, sasa uchumi wetu unaweza ukakua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona madini yatakua kutoka asilimia 5.2 kwenda asilimia 10. Tumeona kilimo kinatakiwa kichangie kutoka asilimia 27, bahati mbaya inaonekana mpaka baada ya miaka mitano hakitakuwa kimechangia sana ukiangalia kwenye kumbukumbu ukurasa 104, lakini niseme tu wazi ni lazima tuhakikishe kwamba sasa hivi masoko yapo, lakini tukiendelea kuzalisha na masoko hayapo tutakuwa tumefanya mchezo wa kuigiza na uchumi wetu hautaweza kupanda kwa sababu, wananchi hawatazalisha sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayoendelea nchini ikiwemo jimbo langu pendwa la Busanda mkoani Geita, mambo kadhaa naomba Wizara iyafanyie kazi; moja, mkandarasi jimboni Busanda aongeze kasi. REA na Geita Nyakanazi Projects.

Pili, transfoma kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo zibadilishwe kwa kuweka zenye uwezo mkubwa, mfano Kijiji cha Nyakagwe na taasisi za umma ziwekewe umeme, kwa mfano shule, zahanati na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, ahadi za Waziri mwaka jana mwezi Julai, 2022 jimboni Busanda zitekelezwe, kama vile solar panel katika Zahanati ya Shilungule Kata ya Busanda, taa za barabarani Mji Mdogo wa Katoro (Kata ya Katoro, Kata ya Ludete na Nyamigota).
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii tena nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii aliyonipatia ya kuchangia katika Bunge hili leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kukubali mpango wa kuirejesha tena Tume ya Mipango. Kwa sababu huko nyuma ilikuwepo, ikaunganishwa na baadaye imerudishwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulisema sana juu ya Tume ya Mipango kwamba, itakwenda ku-centralize mipango yetu na sasa itajulikana nani anatakiwa kufanya nini na wakati gani. Nawapongeza sana Mawaziri wote wawili, Waziri wa Mipango na Waziri wa Fedha. Waziri wa Mipango kwa kutuletea Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka 2024/2025 lakini Waziri wa Fedha kwa kutuletea mwongozo unaotuonesha ni nini kitakwenda kuingia kwenye Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze Mkatibu Wakuu, Mtendaji Mkuu wa Tume ya Mipango na uwasilishaji mzuri uliofanyika kwenye Bunge hili. Pamoja na pongezi hizi, yako mambo mengi ambayo yamesemwa katika hotuba hii. Iko mipango mikubwa imeoneshwa kwenye hotuba hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kujikita kwenye Fungu namba 57 ukurasa wa 27 kinachosema kwamba, Mpango huu utathibitisha Maendeleo ya Kweli yanatokana na Mpango mzuri na nidhamu ya utekelezaji wa mipango hii. Kwa hiyo, kuna hoja ya Mipango na nidhamu ya utekelezaji na hapa ndipo kuna changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki nzima tumekuwa tunaongelea habari ya CAG, ni hoja tu ya nidhamu ya utekelezaji kwamba kuna mahali fulani kwenye nidhamu hatufanyi vizuri sana. Mipango tunayo lakini hatutekelezi vizuri kwa sababu nidhamu yetu iko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kifungu namba 35 ukurasa wa 26, Waziri wa Mipango alitoa Mfano wa Ndugu yangu Lee, kiongozi wa Singapore. Anasema, uwepo wa Mfumo wa taasisi nzuri ni muhimu na inasaidia lakini muhimu zaidi ni kuwa na watu wazuri katika kuendesha mifumo na taasisi ya Serikali. Sasa, hoja yangu hapa pamoja na kwamba aliitoa kama quotation, hawa watu wazuri tunao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto kubwa tuliyonayo ni kwamba, tuna mifumo na taasisi nyingi za Serikali lakini na changamoto ya watu wazuri kama inavyoonekana hapa. tumekuwa tunafanya vetting kila mwaka kwa viongozi mbalimbali lakini baada ya muda tunajikuta kwenye tatizo kwamba, mtu mmoja anaonekana hajafanya vizuri na CAG anatuambia kwamba huyu hajafanya vizuri ameiba bilioni 18, huyu amesababisha loss ya kitu fulani. Kwa hiyo, watu wazuri hatuna. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mpango huu sasa, ni ombi langu kwamba, upande wa elimu watu wa elimu waingize elimu bora ya uraia na uzalendo. Maana inaonekana uzalendo ndani ya nchi hii ni tatizo. Kila anayepewa nafasi anafungua mdomo kwa ajili ya kula badala ya kufungua mikono ili atufanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe sana hili. Tunapokwenda kwenye mipango yetu, watu wa elimu wahakikishe kwamba, mitaala hii ambayo inakuja hivi karibuni inaweza kutufanya kwenda hatua moja mbele kwenye elimu ya uraia na uzalendo ili huu wizi na vurugu zinazotokea hadi Wabunge wamefikia mahali fulani wanafikiria kuwaondoa watu kwenye uso wa dunia, maana yake wanyongwe. Kabla hatujakwenda huko tuwape elimu. Pia tukishawapatia elimu tunajua kuwa matokeo mazuri yatakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana, kiongozi aliyepewa responsibility matrix yake, amepewa nini anachotakiwa kufanya, amepewa KPI yake, vilevile amepewa milestone yake kwamba kama amepotea njia anaweza akajua huku ninakokwenda siko, aende huku. Unashangaa anachokifanya ni kitu ambacho hakuambiwa kwenye ile responsibility matrix yake. Tuna kitu cha kufanya maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa yale ambayo yametekelezwa katika mipango iliyopita. Tunaiona SGR ikiwa sasa inakwenda Lot one iko kwenye hatua nzuri na sasa tunakwenda karibu Lot Five huku. Vilevile, tuna habari ya umeme vijijini ambayo inaendelea kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana, ukiangalia umeme, mchangiaji aliyepita amethibitisha wazi. Nimewahi kufanya kazi viwandani, kama umeme wa kutosha haupo uchumi wetu wa viwanda utadorora kabisa. Hata kama tutaonekana tunapambana kwenye zile hatua nyingine, kama uchumi wa viwanda haujakaa vizuri kwa sababu ya umeme hatuwezi kutoboa. Tutafika mahali fulani tutashindwa tu. Gharama ya kutumia mafuta kuendesha viwanda inaomndoa kabisa ile net profit ya kiwanda, kwa hiyo, niwaombe sana kwenye hii habari ya umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye umeme utagundua kwamba, tuna umeme wa maji megawatt 574. Mpaka sasa tuna umeme wa gesi megawatt kama 1198 hivi, lakini tuna umeme wa mafuta kama megawatt 94.58. Tuna Tungamotaka megawatt 10.5, huu ambao uko gridi karibu megawatt 38, ukiangalia unaona karibu megawatt karibu 1.9 hii storage capacity.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa hivi ukienda kuangalia wanachozalisha watu wa umeme, ni asilimia 50 ya hiyo. Maana yake kwenye Mpango huu tunahitaji kuweka fedha ili hiyo mitambo iliyosimama ikafanye kazi, viwanda vyetu vitembee. Wanasema wameona kabisa maximum demand, yaani umeme wa juu unaotumika kwenye nchi hii kwa Mwezi Agosti, ni megawati 1800. Ukienda kwenye ukweli, tukiwasha migodi yote, tukawasha kwa wananchi wote ambao tumewawekea umeme tutahitaji karibu megawati 5000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaponhgeze kwamba Bwawa la Nyerere litaingia hivi karibuni. Lakini pamoja na kuingia kwa Bwawa la Nyerere, sisi tumesema malengo yetu tunahitaji megawati 10000 kwa ajili ya nchi hii kuanza kuyaona maendeleo. Niombe sana mipango yetu ya umeme iendelee kuwepo na hawa wapewe fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ripoti hii utagundua kwamba, mauzo yetu ya nje ya madini mwaka 2022 yalitoka dola bilioni 3.1 mpaka dola bilioni 3.4. Vilevile, ikaonekana kwenye mauzo ya nje, madini wamefanya vizuri kwa asilimia 56 kwenye mauzo yote ya nje. Kwa hiyo, nilitegemea hapa kwenye madini twende kuhakikisha kwamba tunaingiza fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko vision ya Mheshimiwa Waziri 2030, inayosema kwamba madini ni utajiri lakini vilevile inaonesha kwamba itatuletea ajira za kutosha. Hii vision aliyoisema inahitaji kuingiza utafiti GST unaoitwa High Resolution Airborne Geophysical Survey ambao haujafanyika kwenye nchi hii. Umefanyika kwa asilimia 16 tu. Kwa hiyo, tunategemea kwenda asilimia 50. Niwaombe sana kwenye hili kwamba, huu utafiti upewe fedha na hii ifanyike ili twende kwenye asilimia 50. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukajua kwenye asilimia 16 tumepata dola bilioni 3.4. Je, tukifanya asilimia 50? Kama tumekwishaona haya mafanikio, basi haya mafanikio tuyaongezee nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme, kule kwangu wanachimba madini. Maeneo yote yanayoleta haya madini, barabara zake ni mbovu. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri anayeshughulika na barabara (ujenzi wa miundombinu), katika nafasi hii tuliyonayo sasa ya kutoa mapendekezo kwenye hili, zile barabara zijengwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeisema sana barabara ya kutoka Geita kwenda Kahama, inapita kwenye migodi katika majimbo matatu. Hawa watu wanabeba Carbon, hawa watu wanabeba magogo, hawa watu wanabeba selenide, ili waongeze kwenda na kurudi kwa urahisi ni lazima watengenezewe barabara ili wazalishe mara tatu ya hiki ambacho leo tunakiona leo. Kama hatutafanya hivyo maana yake uzalishaji wetu hautapanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara inatoka pale kwangu Katoro kuelekea Jimbo la Bukombe, linapita kwenye migodi zaidi ya sita hadi saba. Niombe sana barabara hii itengenezwe. Haitengenezwi kwa ajili ya kuwafurahisha wale watu. Inatengenezwa ili iweze kuwafanya wale watu wafanye kazi zao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kilimo, mwaka 2022 tumetenga zaidi ya bilioni mia tisa tisini na kitu lakini tunaona kabisa sekta ya kilimo cha umwagiliaji imekwenda kutoka hekta 300 mpaka hekta 800. Lengo letu ilikuwa ni hekta milioni 1.2 bado kuna 400 bado hatujaifikia kwa miaka hii mitano. Niwaombe sana kwenye utekelezaji wa bajeti hii, kwenye mapendekezo yangu fedha ipatikane ya kuongeza kwenye eneo hili la umwagiliaji ambalo linaajiri watanzania wengi ili waweze kuchangia pato la Taifa kwa kiwango kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ninayotoka mimi kuna Ziwa Victoria lakini maji yake hayajatumika. Yakitumika ninaamini tutazalisha kuliko inavyoonekana leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii katika kilimo hiki hiki ambacho tunakiona kama ni cha mchezo mchezo, inaonekana tulizidi kwa asilimia 124. Kwa hiyo, tulizidi. Maana yake ni kwamba, tukiwawezesha zaidi tutapata hata asilimia 200. Kwa kuwa kilimo ni biashara sasa itatufanya hawa watu wetu watakula na tutauza mazao yetu nje. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana…

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hoja ya uvuvi. Ndugu yangu Jirani hapa Mheshimiwa Mwijage asubuhi alisema kwamba, mpaka sasa uvuvi wa vizimba tuna metric tani 18000, wenzetu wa Uganda wana metric tani 120000. Egypt wana tani milioni moja kama na laki mbili. Nilikuwa nafanya hesabu ya kawaida tu. Leo tukiweka tukawa na metric tani milioni moja, tunauwezo wa kutengeneza trilioni tano kwa mwaka. Trilioni tano hii itakwenda kufanya kazi kubwa, tunaogopa nini kwenye potential kubwa ya uvuvi kuingiza fedha. Tunaogopa ni kwenye potential kubwa ya mifugo kuingiza fedha? (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Tumaini Magessa, muda wako ulikuwa umekwisha. Naomba tafadhali umalizie.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa fursa hii ya kuweza kunipatia kuchangia katika Mpango huu wa Tatu wa miaka Mitano. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa mpango mzuri uliojikita kutoka kwenye document takriban kumi na moja ambazo amezi-refer, ikiwemo Dira ya Maendeleo ya Taifa ya 2025, ikiwemo Agenda 2063 ya Afrika, lakini na nyingine nyingi mpaka hizo document kumi.

Mheshimiwa Spika, binafsi mimi nitajikita katika maeneo mawili tu kwa sababu ya muda. Eneo la kwanza ni la elimu, ambalo liliguswa na mchangiaji wa kwanza au wa pili wa siku ya leo.

Mheshimiwa Spika, ukurasa naamba 25 wa mpango huu unaonyesha kwamba mwaka 2014 Tume ya Mipango ilifanya utafiti wa soko la ajira na ikaja na majibu kwamba ujuzi wa wale watu ambao wanapata elimu ndani ya nchi hii ulionekana ni pungufu kulingana na mahitaji ya waajiri. Maana yake waajiri kwenye viwanda, kilimo na sehemu zingine. Ukaja na mapendekezo kwamba tunatakiwa tuwekeze, kwenye mpango huo huo, wanasema tuwekeze mara tano ya uwekezaji uliokuwepo mwaka 2014 ili kuweza ku-fill hiyo gape ambayo inaonekana kwenye elimu tuliyonayo.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi nishauri; ukurasa namba 73 umekuja na majibu kwenye mpango huu huu. Kwamba tunatakiwa tuguse elimu ya msingi kwa kitu kinaitwa SATU (Sayansi Teknolojia na Ufundi); yaani wanategemea kwenye SATU tuguse hiyo primary; lakini tuguse kitu ya T and M kwenye elimu ya vyuo vikuu kwenye mpango huu. Lakini elimu tuliyonayo sasa ni competence-based education; ambapo competence-based education tunatakiwa tunapotengeneza mitaala yetu tuwe makini.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, ninategemea kabisa kama tulitakiwa kujaza huo udhaifu ulioonekana hapo tunatakiwa hawa waajiri na mazingira yetu ya kazi yahusike, tujue ni competence gani tunahitaji kwenye watu wetu. Kwa mfano, tunamuhitaji mtu ambaye atakwenda kulima maana yake competence ni kilimo; sasa ile principal outcome ya hiyo curriculum tunategemea ituletee mtu ambaye atakuwa na elimu ya kilimo, halafu twende kwenye hizo enabling kwamba tunakwenda kumu-enable nini ili aje ya hiyo principal outcomes.

Mheshimiwa Spika, sasa ninaona kabisa kuna mahali fulani Wizara ya Elimu huenda inachukua kumbukumbu za knowledge based na kutengeneza curriculum na hatimaye ndiyo sababu hatuwapati hao ambao tunawahitaji. Kwa sababu kama tunahitahi na tunaujua mwisho wetu tunashindwaje kutengeneza process ya katikati ili tuwapate hao wataalam? Kwa hiyo niishauri Wizara ya Elimu waangalie competence gani tunahitaji kwenye eneo hili, baadaye waende kwenye principal outcome waende sub-enabling na mwisho wa siku tutakuwa tunaweza kupata ability ambazo tunazihitaji kwa watu wetu. Tutapata hicho tunachohitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niguse viwanda. Mimi niseme tu ni-declare interest, mimi ni mhandisi; tunatatizo kwenye viwanda vyetu. Ukisoma kwenye document ya Mheshimiwa Waziri ya mpango huu ukurasa namba 68 unaonesha tutakuwa na viwanda vya ku-process; lakini umeonyesha mambo mawili kwenye ukurasa wa 68. Unaonesha kwamba ni lazima tuwe na mali ambazo tunaziuza nje ambazo zipo- process. Lakini ya pili ulionesha kuwa lazima kuwe na political will, kuwe na utashi wa kisiasa wa kufunga mikataba ambayo ina faida kwa nchi, kwenye ukurasa wa 68; ni document hii ambayo ninaizungumzia hapa.

Mheshimiwa Spika, sasa shida ninayoiona tunapoenda ku-process kwenye viwanda vyetu; kwa mfano viwanda vya alizeti, hakuna kiwanda cha alizeti kinachota double refined oil nchi nzima, tunatoa semi refined kila mahali, na haya ndiyo mafuta ambayo kila Mtanzania amekula. Kuna mahali fulani hata ukimuona mtu anachangangia anachemka unajua hii ni semi refined ilimu- affect tangu utoto mpaka leo ndiyo sababu anahemuka. Kwa hiyo kuna mahali ambapo tunatakiwa sasa tutengeneze double refined ili watu wetu wale mafuta yaliyosafi (quality food) lakini tunachotengeneza ni semi refund na watu wote wanakula semi refined.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme, tunatakiwa tuongeze ujuzi kama tulivyosema. Kuna njia mbili ya kutengeneza mafuta kwanza ni press; yaani ku-press you press by hydraulic au you press by expeller machines kuna machine kumal, kuna machine za VIP zinafanya hiyo pressing. Hiyo teknolojia ya zamani, teknolojia ya sasa ambayo itatutolea mafuta mengi ni solvent extraction ambayo nchi nzima hakuna mahali ambapo tunafanya solvent extraction tunafanya pressing tu. Na ili u-press mafuta kutoka kwenye mbegu zetu lazima utumie motor kubwa na gharama yake inakuwa kubwa. Kwenye solvent unatumia chemicals tutaenda kufanya double refine tutakuwa na mafuta yaliyo safi. Nchi nzima sasa ina mafuta yanatoka Uturuki wanatumia solvent extraction, kwa nini sisi tusiingie kwenye teknolojia hiyo ili tuweze kupata mafuta?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kuna habari ya gape ya ujuzi ambayo tunatakiwa kwenye viwanda na biashara sasa waangalie gape hiyo mahali gani kwenye uhandisi tunaiondoa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzunguzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia Wizara ya Mifugo na Uvuvi. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu vile vile kunipatia nafasi hii. Niwapongeze sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na wataalam kwa bajeti nzuri waliyoiwasilisha leo.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme mambo machache katika bajeti hii. Bajeti ya Uvuvi inaonekana kwenye utekelezaji, hela ya Serikali iliyokwenda mwaka 2020 ni asilimia 30 tu. Kwa hiyo, naishauri Serikali iongeze kupeleka pesa kwa ajili ya utengenezaji wa bajeti hii kwa sababu inawagusa sana wananchi wetu. Vile vile kwenye bajeti hii upande wa mifugo bado pesa iliyokwenda ni kidogo. Kila unapoangalia kwenye bajeti hizi utagundua mchango wa Serikali kwenye mchango ule ambao Serikali inatakiwa itoe, kwenye bajeti nzima ya nchi ni kama 0.08. Kwa hiyo, ni ndogo, haifiki hata asilimia 1 na hasa hizi za uvuvi na mifugo ni kama 0.03. Ni ndogo sana. Kwa hiyo, kama tunatarajia maendeleo makubwa na uchangiaji mkubwa wa pato la Taifa, tunategemea bajeti hizi ziongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Waziri, kwenye uvuvi safari hii development budget ameiongeza mara saba; seven point something ambayo inaonesha kabisa kwamba kuna vitu vikubwa kwenye uvuvi vitakwenda kutokea japokuwa kwenye mifugo bado development budget ni ndogo kwa hiyo, naamini hakutakuwa na mabadiliko makubwa sana kwenye Sekta ya Mifugo.

Mheshimiwa Spika, niungane na wewe ulivyosema NARCO ni kama imeshindwa hivi. Pamoja na kushindwa nitoe ushauri kwamba tunatakiwa tuunde sasa kitu kinaitwa Livestock Development Authority. Katika hilo, tukishakuwa na authority hii wao maeneo yao sasa kama wataya-surrender wayaache kwenye Halmashauri na Halmashauri iwape watu binafsi na vikundi mbalimbali kwa ajili ya kuhakikisha kwamba uzalishaji huu unaweza ukaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kuunda hiyo Livestock Development Authority, tufanye kama Waganda. Tuwe na Dairy Development Authority ambayo itashughulika na maziwa na nyama. Kwa sababu, mpaka sasa hivi haya maziwa tunayosema yamezalishwa hapa yameshindwa kuuzwa nje kwa sababu hatuna chombo kinachoshughulika na haya. Kwa hiyo, tuunde chombo hicho, Dairy Development Authority ambayo itakuwa inashughulika na hii. Tutakapokuja kwenye bajeti nyingine, watatupa taarifa sahihi ya nini wameanzisha katika kuingia kwenye Soko la Kimataifa kuuza maziwa.

Mheshimiwa Spika, kitu kingine ambacho nataka nikizungumzie kwenye mifugo ni nyanda za malisho. Tunataka kufuga na sisi tupo atika tatu bora Afrika kama wafugaji wa ng’ombe. Mifugo hii tusipokuwa na malisho ya kutosha imekuwa ikisababisha mifarakano mikubwa katika jamii, wananchi wanagomba kati ya wakulima na wafugaji. Ugomvi huu unaotokea kati ya wakulima na wafugaji ni kwa sababu hakuna nyanda za malisho na hatujapanga matumizi bora ya ardhi kwa utaratibu mzuri ambao unaweza kutufikia nyanda za malisho wasigusane wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe rai hapa kwamba tunazo sheria za kutosha. Tunayo Sheria Na.5 ya Mwaka 1999 ambayo inavikabidhi vijiji ardhi, inakuwa ni mali ya vijiji. Pia tunayo Sheria Na.7 ya Mwaka 2007 inayoshughulikia matumizi bora ya ardhi. Tunayo Sheria Na. 13 ya Mwaka 2010 inayozungumzia habari ya nyanda za malisho. Tuone ni namna gani bora tunaweza kufanya wakulima na wafugaji wasigombane kwa sababu hii ni kama Wizara moja. Kila mmoja azalishe lakini kwenye ardhi hii tuliyonayo.

Mheshimiwa Spika, nitoe ushauri tu kwamba tunapokwenda kwenye utekelezaji wa haya ambayo tunayafanya mwaka huu tuangalie namna gani tutaenda kushughulikia nyanda za malisho maana matumizi bora ya ardhi tuliyonayo yafanyike kwa wingi ndani ya maeneo tuliyonayo. Bahati mbaya sana jana ilikuwa Wizara ya Ardhi. Kwa hiyo, najua hili wao wanahusika na Wizara ya Mifugo nayo wanahusika kuhakikisha kwamba nyanda za malisho zinakuwepo ili ugomvi huu tunaousikia kila siku upungue. Migogoro ya ardhi inafifisha sana ukuaji wa Sekta hizi.

T A A R I F A

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa unapewa.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba tatizo la Nyanda za Malisho halitokani na kutokuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi kwa sababu vijiji vingi tayari vimeshapimwa. Kwa mfano, katika Jimbo langu la Longido kati ya viji 49, 30 vimeshapimwa na vina mpango wa matumizi bora ya ardhi, lakini kuna mashindano kati ya Wizara na Wizara. Wakati Wizara ya Mifugo haihangaiki ku-secure na kuhifadhi nyanda zake za malisho, maliasili wao wako kazini kutafuta nyanda za malisho za kuchukua na kuongezea kwenye hifadhi.

SPIKA: Taarifa hiyo Mheshimiwa Magessa.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naipokea. Inaonekana tena kwamba kuna habari tena ya wanyamapori na siyo ya wakulima na wafugaji. Naipokea Taarifa hiyo. Najua kabisa Mkungunero pale kuna shida hiyo na kwa ndugu yangu Ngorongoro kuna shida hiyo. Hizi Wizara zifanye kazi kwa pamoja kwa sababu ni Wizara ya Serikali. Kwanini zinashindana? Shida yetu kubwa ni kumtumikia mwananchi, hatuna haja ya kushindana. Nafikiri hili limeshazungumzwa sana kwamba Wizata zikutane kwa pamoja kujua nani anafanya nini na wakati gani ili wananchi waweze kupata maendeleo? Naomba niipokee Taarifa hiyo. Naikubali Taarifa yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme pamoja na ufinyu wa malisho kuna upungufu wa majisafi na salama kwa ajili ya mifugo hii. Kuna upungufu mno wa maji na mabwawa. Ningeomba sana mabwawa yaweze kuongezwa. Vile vile kumekuwepo na shida katika Sekta hii, kuna uwepo wa soko holela na bidhaa za madawa na vifaatiba vya mifugo. Sasa watu wanaleta tu dawa, badala ya kutusaidia ng’ombe wetu wakati fulani ng’ombe wanakufa. Pia kuna mwamko mdogo wa ufugaji wa kitaalam kwa kuzingatia idadi sahihi ya mifugo katika maeneo ya malisho. Hili nalo, tuna ng’ombe wengi lakini je, elimu imetolewa ya kutosha kuhakikisha kwamba wananchi wetu sasa wanaweza kufuga kitaalam badala ya hii ambayo inafanyika sasa hivi, inafikia mahali fulani watu wanagongana. Naamini kabisa hili likitolewa elimu, changamoto hizi zitapungua.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye uvuvi sasa. Mimi kwenye maeneo ninayotoka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, hii kengele ya kwanza?

SPIKA: Ndiyo?

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo ninayotoka nina mialo yapata karibu saba. Nina mwalo sehemu moja inaitwa Butunde, Kasamwa, Kageye, Bukondo, Busaka, Chankorongo na Kabugozo. Maeneo yote haya ni sehemu ambayo nategemea wavuvi waweze kufanya kazi na kupata maisha. Bahati mbaya sana katika haya mazingira ya uvuvi, hawa wamekuwa wanafanya uvuvi huria tu. Akichukua mtumbwi wake asubuhi, anakwenda anakuja na samaki watatu au watano usiku mzima. Tunahitaji kuwawezesha hawa watu kwa kuwapa elimu na kuwafundisha.

Mheshimiwa Spika, kwenye kilimo tuna mashamba darasa, sijui kwenye uvuvi tutaita nini? Sijui tutaita uvuvi darasa, sielewi tutaita kitu gani? Ila tuwe na namna ambavyo hawa wavuvi wanaweza wakafundishwa. Sasa hivi dunia imehamia kwenye uvuvi wa vizimba. Nilimwona ndugu yangu mmoja alisimama hapa, ni mtaalam kwenye cage hizi (vizimba). Nimejaribu kuangalia kwenye maeneo yote hayo niliyoyataja, hakuna kizimba hata kimoja.

Mheshimiwa Spika, niseme tu, kwa sababu tuna kituo kikubwa kilichoko pale Chato, naamini kwamba kituo hicho sasa Wizara inaweza kukitumia kutusaidia sisi maeneo hayo kupata vizimba; kwanza vije vizimba vya mfano watu waone kinachofanyika; na wapatikane hao Maafisa Ugani wa kufundisha hiyo kazi kwa sababu hatunao sasa, lakini tuoneshe mfano halafu baadaye watu waingine kwenye vizimba. Watu wanasema kuna maeneo mengine yamechukuliwa kama breeding area, eneo tu la kufanya watu wazalie, lakini nafikiri tukifuga samaki maana yake hatuzuii breeding hiyo ambayo inafanyika sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naombe sana Wizara watusaidie kwa sababu tuna changamoto kubwa ambayo inaonesha ili uweze kuingia kwenye vizimba hivyo, inabidi ufanyiwe environmental impact assessment. Hii ni gharama kubwa. Inatakiwa TAFIRI waingie hapo, nao wana tozo yao; halafu Kata, Kijiji na Wilaya nayo ina tozo yake. Napendekeza sana, TAFIRI ambao wanashughulika na mambo ya samaki hawa ndio wachukue tozo moja tu. Wakishachukua wao ndio watai-distribute huko kwenye environmental impact assessment.

Mheshimiwa Spika, badala ya kuonekana huyu mtu mmoja mvuvi masikini anakwenda kulipa hizi na gharama yake ni kubwa, zinakwenda karibu milioni 10, ni nani mvuvi wa kawaida ana uwezo wa kuzilipa? Maana yake lazima Serikali iingie kuhakikisha kwamba tozo hizi zinapungua ili wananchi wa kawaida waingie kwenye hivyo vizimba na mwisho wa siku tutaona maendeleo yamekuja. Tumepata umeme sasa. Umeme huu utatumika wapi kama uvuvi wenyewe utaendelea kuwa wa mtu mmoja mmoja. Umeme huu utumike vizuri kuona viwanda vidogo vidogo vya samaki ili mapato haya yaweze kuongezeka.

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa Waziri na Naibu Waziri na Naibu Waziri wanajua, Kituo chao cha Nyamirembe kina uwezo wa kufanya kazi kubwa kwenye maeneo hayo na tukaona matokeo makubwa. Wananchi wetu tunategemea mifugo iliyoko. Kwa mfano, mifugo iliyoko Jimboni Busanda, mingi inabidi ipelekwe Misenyi. Sasa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii nami nipate nafasi ya kuchangia kwenye hotuba hii ya Makadirio ya Bajeti ya Mwaka 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda sana kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi aliyonipatia kuweza kuzungumza tena siku ya leo katika bajeti hii kuu. Mwanzo kabisa niipongeze sana hotuba ya bajeti kuu iliyosomwa hapa na Mheshimiwa Waziri wa Fedha, akimwakilisha Rais na mimi naunga mkono hoja hii kwanza kabla hata sijazungumza kwa sababu yapo mambo mengi mazuri yaliyooneshwa kwenye hotuba hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shabaha za uchumi zilizoelezwa kwenye hotuba tunayoizungumzia hapa ni kuongeza kasi ya ukuaji wa kiuchumi kutoka asilimia 4.7 tuliyokuwa nayo kwenda kwenye asilimia 5.6, lakini vilevile imeonesha wazi kwamba tunataka kwenda kwenye asilimia 6.3 mwaka 2023 lakini mfumuko wa bei tunataka uwe kati ya asilimia Tatu (3) na asilimia (5) kwa mwaka huu. Vilevile mapato ya ndani tunataka yaongezeke na mapato ya kodi tunataka yaongezeke sasa inaonekana kuna kazi kubwa sana ya kufanya kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, yapo maeneo mahsusi ambayo matarajio yetu makubwa ya ukusanyaji wa kodi hii yanatakiwa yawafikie nayo ni barabara za mijini na vijijini TARURA, kuna maji safi na salama, kuna bima kwa wote, kuna habari ya shule tunatakiwa tujenge shule, ukienda kwenye afya tu unaona kuna maboma ya zahanati karibu 8,000 yanahitaji kukamilishwa. Lakini ukienda kwenye vituo vya afya hotuba hii inaonesha kuna vituo vya afya zaidi ya 1,500 vinatakiwa kukamilishwa kwa hiyo ni dhahiri kwamba tunahitaji fedha ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia vyanzo vyetu vya fedha ukiviangalia vya mwaka jana na mwaka huu vimebadilika kidogo sana japokuwa inaonekana kuna hii tumezoea kusema indirect tax, hii kodi ya LUKU iliyoongezeka na inayotoka kwenye LUKU mwa maana ya majengo (property tax), lakini na hii nyingine iliyoongezeka kupitia kwenye mitandao ya simu kwa matumizi ya siku tulizonazo. Ukiona kuna Trilioni Mbili imeongezeka hapa lakini tukiangalia kwa uhalisia vyanzo vile ukiangalia kwa percentage tumeongeza tu mapato ya ndani ya kodi kwa asilimia 72 vingine vimebaki kama vilivyokuwa tumepunguza kule kwenye mikopo ya ndani na ya nje.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hoja kubwa tuliyonayo ni ukusanyaji wa mapato, kwamba kazi kubwa tuliyonayo hapa ni ukusanyaji wa mapato lakini ukiangalia mikakati iliyowekwa kuna ile EFD Management System, kuna habari ya kuhakikisha kwamba ile blue print inatekelezeka na uwekezaji mwingine ambao tunauona kwenye maeneo hayo. Binafsi niishauri sana Serikali iongeze nguvu katika ukusanyaji wa kodi ni kweli tumesema tutakusanya kodi sahihi kwa sheria sahihi.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuongeze sana eneo hilo kwa sababu kama hatutakusanya kodi ya kutosha haya ambayo tunayaona leo kama hotuba nzuri sana tutakapokutana tena kuijadili tutaanza kulaumiana sisi kwa sisi, kwa nini. Nina mfano mzuri wa mwaka jana, tulikuwa na hotuba ambayo inaonekana imeandikwa kama nilivyosema inatofautiana kiasi na hii lakini nikienda kwenye kilimo, mfano kilimo tu development budget iliyotekelezwa mwaka jana ilikuwa kama 30 percent sasa tunataka kwenda mbele tunataka kuhakikishe kwamba tunakwenda kufanikiwa kusogeza uchumi kutoka asilimia 4.7 kwenda kwenye asilimia
5.6. Hoja ambayo ninaiona kwenye bajeti yetu hapa ambayo ningependa nitoe ushauri kwa Serikali zile sekta ambazo ni za uzalishaji kwenye bajeti hii hazina fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano, ukiangalia percent ya hiyo Bilioni 294 ya kilimo kwenye development budget nzima utagundua ni 0.08 ambayo ni kama asilimia 0.8 haifika hata asilimia moja lakini hiyo inaajiri watu asilimia 65 wa nchi hii na tunataka sasa twende mbele, kama mchango wenyewe ndio huo yaani unataka kitu fulani kitokee lakini input yako ni ndogo kiasi hicho maana yake hata hawa Mawaziri wa Kilimo tulionao watajitahidi kadri wanavyoweza lakini hawataweza, kwa sababu hawana fedha ya kutosha wana mipango mingi tupate mbegu, wana mipango mingi tuanzishe mashamba darasa, tuanzishe tulime Alizeti kwa fedha hii tuliyonayo Bilioni 294 ambayo haifiki hata asilimia moja haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tufikirie ninajua tayari bajeti ipo mezani tutakwenda kuitekeleza lakini matokeo yatakayokuja huko mbele hayawezi kuwa ya kushangaza sana, hatutasogea sana kwa sababu asilimia 65 ya watu ambao tunagemea tuwawezeshe hawataweza na bahati mbaya sana hata viwanda vinawezeshwa na uzalishaji wa kilimo, sasa kilimo hakijawezeshwa vya kutosha maana yake na viwanda havitafanya vizuri, kwa hiyo mwisho wa siku tutakapokuja kuzungumza hapa tutagundua hata hao tunaotaka kuwatoza kodi watakuwa wachache. Kwa mfano, Halmashauri nyingi nchini zinakusanya ushuru wa mapato kutoka kwenye mazao, sasa kama fedha iliyokwenda kwenye kilimo ni kidogo tutakusanya nini kutoka kwenye Halmashauri? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawatakusanya sana watakwenda hapo hapo, mwaka huu tumeongeza Bilioni 200 kwenye malengo yetu Je, watazitoa wapi? Kwa sababu hatujachakata kuwaanzishia ili waweze kufanya uzalishaji mkubwa na tukusanye hivyo, vivyo hivyo kwenye uvuvi, vivyo hivyo kwenye mifugo, bado kile ambacho tumekitoa ni kidogo kwa hiyo tuangalie kile ambacho tunakiweka mahali kwa ajili ya kuzalisha, tukiweka kidogo tutapata kidogo na mwisho wa siku tuhakikishe kwamba development budget tunayoipeleka kule iende kama tulivyo i-plan mwaka kesho tutaanza kuulizana tulipanga iende asilimia 100 imekwenda asilimia 25 matokeo yake tutakuwa hatujafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee sehemu ya pili ambayo nilitaka kuizungumzia eneo la madini, tunategemea madini yachangie tufike kwenye pato la Taifa asilimia 10, changamoto ambayo ninaiona sasa miundombinu tuliyonayo binafsi nimekuwa ninazungumzia barabara ya kutoka Geita kwenda Bukoli kupita Runguya kwenda Kahama, hii barabara inapita kwenye migodi, haipitiki sasa! Kama haipitiki hiyo ndio hata makinikia yanayoulizwa humu ndani yanapita barabara hiyo, sasa tutakwendaje kufanya hii shughuli ambayo tunataka kufanya wakati miundombinu haipo? Lakini niseme…

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Magessa kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi.

T A A R I F A

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilipenda nimpe taarifa mzungumzaji kwamba barabara hii inayotoka Geita - Bukoli, Bukoli - Kakola, Kakola-Kahama ni barabara ambayo kimsingi iliahidiwa kupewa kiasi cha dola milioni 40 na Mgodi wa Bulyanhulu, fedha hizo bado hazitolewa na Serikali sijui ni kwanini lakini pia barabara hii imekuwa ni adha toka makinikia yameanza kusafirishwa na magari haya yanayobeba makinikia yanatembea makundi kwa makundi gari zisizozidi 40 vumbi limekuwa ni kubwa sana, kwa ruhusa yako…

NAIBU SPIKA: Subiri kwanza unamuongezea mchango kwenye hoja ipi aliyokuwa anazungumza?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya barabara inayotoka Geita - Bukoli…

NAIBU SPIKA: Yeye alikuwa amemaliza kuzungumza hoja yake.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, alimaliza!

NAIBU SPIKA: Au wewe umeamua umalizie ili yeye asimalizie mchango wake?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, alimaliza na nilitaka kumuongezea kwa sababu kwa ruhusa yako nimekuja na sampuli ya vumbi limo kwenye begi humu, nilitaka uniruhusu niweze kumkabidhi ili aliachie humu vumbi aone namna gani wananchi wa Bulyanhulu…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi naomba ukae.

Waheshimiwa Wabunge, kuna nyakati mtu anakuwa ana mtiririko fulani hivi wa mchango wake usimkatishe kabla hajaweka nukta, ukimkatisha maana yake kuna jambo labda anakosea unataka umrekebishe labda yeye kasema 10 kumbe ni tisa, sasa wewe unamkatisha ili wewe ndiyo useme vizuri jambo lake kabla Mbunge hajasema yeye hoja yake, yaani unakuwa kama unaonesha kwamba yeye hajaweza kumalizia hoja yake vizuri wewe ndiyo unataka umsaidie, sasa haikai vizuri kwa hiyo tusubiri awe anamaliza sentensi yake ndiyo wewe uingie hapo.

Waheshimiwa Wabunge, mtu anayetaka kuchangia jamani sisi huwa tunawapa nafasi kama kwenye orodha haupo andika hapa mbele utapewa fursa ya kuchangia, ukimkatisha Mbunge mwenzio hizi zinakaa kwenye Taarifa Rasmi za Bunge kila tunachokizungumza humu ndani, sasa sisi wenyewe tuwekeane mazingira mazuri ya kuachiana nafasi za kuchangia kama hakuna jambo ambalo kweli unataka wewe kuchangia kwenye hiyo taarifa unayotaka kuitoa, maana nimeona wengi huwa unataka kuiseme barabara yako basi unasema hilo lililoko huko na huku hivi hivi ahaha!

Mheshimiwa Magessa malizia mchango wako.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa hayo ambayo umeyasema. Niseme tu naendelea na hiyo barabara kwamba kumekuwa na mazungumzo ambayo umri wake ni zaidi ya miaka minne ya hiyo dola elfu 40 ambayo wadau kwa maana ya Barrick waliridhia baada ya mazungumzo barabara hiyo ianze kujengwa lakini nashangaa miaka minne Wizara ya Fedha, Wizara ya Madini wanazungumzia nini kwa miaka minne? Kwa hiyo kuna mahali fulani wananchi wanakaribia kupata mafanikio lakini mazungumzo yanachukua muda mrefu sana, kwa hiyo barabara hii imekuwa sasa vumbi kama alivyokuwa anataka kuchangia ndugu yangu hapa, vumbi lake linatisha. Leo hii ukimkaribisha mgeni kutoka Geita ukamwambia njoo Dodoma unitembelee akifika hapa utafikiri umekutana na ninja alitaka kuvamia mahali kwa sababu pua zote zitakuwa zimejaa vumbi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niseme wazi kama makinikia yanapita hapo na dhahabu kuchenjua tunategemea ipite hapo nimshukuru nimpongeze sana Mheshimiwa Rais amefungua na amezindua kiwanda cha kusafisha dhahabu refinery pale Mwanza wamesema kuna sehemu itakuwa kwa ajili ya kukopesha wachimbaji wadogo, sasa hii dhahabu tutaitoaje huko Runguya tutaitoaje huko Msalala, tutaitoaje huko Geita ili iende Mwanza? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama barabara tu inazungumziwa miaka minne na wadau wanataka kuweka fedha lakini haieleweki inaishia wapi, kwa hiyo niseme wazi ili tuendelee kuzalisha vizuri na dhahabu iendelee kwenda wamesema kuna kilo 400 kwa siku inatakiwa kilo 400 lakini baadaye inatakiwa kilo 900, kilo 400 ni karibu nusu tani, lakini kilo 900 ni karibu tani moja itapatikana wapi hii, lakini nijielekeze tena kwenye kodi…

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii, lakini nikushukuru wewe kwa kuniruhusu kuwa mchangiaji wa tatu wa Wizara hii ya Madini. Nimpongeze sana Waziri na Naibu wake Profesa Manya kwa kazi kubwa ambayo wameifanya kwa bajeti nzuri ambayo wametuletea hapa. Bajeti ambayo inatuonyesha wazi kwamba, lengo lake ni kututoa katika mchango wa Taifa wa asilimia 5.2 kwenda kwenye asilimia 10 Mwaka 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa malengo ni makubwa, ni karibu mara mbili, mchango wa Taifa unatakiwa kuwa karibu mara mbili, labda nirudi kwenye bajeti yenyewe sasa. Bajeti iliyopita, tuliweka bajeti ya shilingi bilioni 62 na katika matumizi ya kawaida tulibajeti bilioni 54, lakini bajeti ya maendeleo ilikuwa bilioni 8.5. Ukienda kwenye utekelezaji wake, utaona ile bajeti ya matumizi ya kawaida ni karibu inatekelezwa kwa asilimia mpaka mwezi Machi ilikuwa karibu asilimia 112, lakini bajeti ya maendeleo imechangiwa tu kwa shilingi bilioni 1.7. Hii inaonyesha kwamba imechangiwa kwa asilimia 22 tu kwa malengo tuliyokuwa nayo. Ikionyesha kwamba nia yetu ni njema kwenda huko tunakotaka kwenda, lakini mchango wa bajeti ya maendeleo wa Serikali kwenye Wizara hii ni mdogo, asilimia 22, lakini malengo yetu ni kwenda mara mbili. Kwa hiyo, kuna tatizo hapa wanatakiwa wawezeshwe sawasawa na malengo tuliyojiwekea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda mwaka huu, tuna bilioni 66 kama bajeti; matumizi yetu yatakuwa bilioni 51.8, bajeti ya maendeleo bilioni 15, imekuwa kama mara mbili hivi. Sasa ukijiuliza kwenye trend kama mwaka jana tumetoa 1.7 bilioni, je mwaka huu tutatoa ngapi? Kwa hiyo, kwa ushauri wangu hapa kwa Serikali ni kuhakikisha kwamba, tunatoa pesa ya kutosha kwenye bajeti ya maendeleo. Bila hivyo tutaendelea kuona ukuaji mdogo kwa sababu ni lazima input iwe kubwa ili tuone matokeo makubwa. Pamoja na ukuaji huo ukiangalia mwaka 2017, pato la Taifa lilichangiwa kwa asilimia 4.8, lakini 2010 asilimia 5.2. Sasa tunatakiwa kuingiza pesa nyingi kwenye bajeti ya maendeleo ili tuweze kuona maendeleo ambayo tunayatarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye uchimbaji unaoendelea pamoja na ukuaji huu niliouona. Tunakusanya maduhuli; ukiangalia kwenye ukusanyaji wa maduhuli, tumekusanya maduhuli mengi maana yake ukiangalia kwenye bajeti hii, utaona kwamba rasilimali watu tulioingiza huko ni kubwa ndiyo sababu, bajeti ya kawaida ya matumizi ni kubwa sana kuliko bajeti ya maendeleo. Sasa je, kwa nini tusiji-involve kwenye teknolojia kupunguza hiyo bajeti ambayo ni ya matumizi ya kawaida iende kwenye bajeti ya maendeleo ili tuweze kukimbia kwa haraka zaidi? Kwa hiyo, kuna kazi kubwa ya kufanya hapo, kwa mfano, mwaka huu inaonekana imepungua kidogo kama bilioni tatu na tukaongeza kwenye bajeti ya maendeleo. Je. Kwa nini tusiendelee kuipunguza hii kwa ku-employ teknolojia, ili tuhakikishe kwamba sasa tunaweza kukimbia zaidi kuliko tunavyokwenda sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine hawa wakusanyaji wa maduhuli, nitawaonyesha uzoefu wa huko ninapotoka Jimboni Busanda. Asubuhi tunapoamka, samahani nitatumia neno zito inawezekana wengine wasilijue, kwenye illusion, mahali ambapo tunakwenda kuingiza carbon zetu kuchenjua dhahabu. Utakuta illusion ziko labda 10 au 15 lakini group la kudhibiti la kwenda kukusanya maduhuli ni moja. Kwa hiyo, utakuta illusion namba kumi itafikiwa saa tisa jioni kwa hiyo, ni hoja yangu kwamba ushauri wa Serikali waongezwe hii timu ya ukusanyaji wa maduhuli huenda tukakusanya kuliko tunavyokusanya sasa. Wasiendelee kuwa wale wale kwa sababu, tumekusanya kidogo kwa sababu na wale tuliowaweka kwenye utaratibu huo ni wachache. Tuwaongeze hawa ili watu wetu wasiwe na shida ya kuwapata wakati wa ukusanyaji wa maduhuli haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo nataka nishauri, tumesema kuna ujenzi wa hawa wachimbaji wadogo wadogo, tuwawezeshe wachimbaji wadogo, hili nimekuwa nalisema mara nyingi, ni wapi wanapowezeshwa hawa wachimbaji wadogo? Tulisema STAMICO wanafanya kazi hii, wachimbaji wetu wadogo kwa sababu ya teknolojia na utafiti mdogo tuliokwishaufanya ndani ya nchi kwenye madini, wamehamia sasa kuchukua nafasi ya wafugaji kuishi nomadic life. Wakisikia leo madini yanasemwa yako Singida, wanakimbia Singida; wakisema yako Songea, wanakwenda Songea. Je, sisi hatuna map yetu inayoonyesha kwamba dhahabu iko wapi, helium iko wapi, makaa ya mawe yako wapi, ili hawa watu wasihamehame kwa mtindo huo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho nataka niseme, kuna mahali watu wetu wanachimba uchimbaji mdogo, lakini dhahabu inatakiwa ichimbwe labda kwa wachimbaji wakubwa, inapatikana labda kilometa moja. Tumefanya utafiti huu ili tuwaambie wasiendelee kuchimba hapo dhahabu iko mbali hawataweza kuchimba kama wachimbaji wadogo wakaipata?

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nafikiri niishauri Serikali, tutengeneze Mfuko wa Madini kwa ajili ya wachimbaji wadogo, ili vifaa vya uchimbaji vipatikane mahali fulani wanapoweza kuazimwa au wanapoweza kulipia, kwa sababu, sasa hivi hatuna mahali. Ukimwambia mtu aanze kuchimba leo dhahabu au aanze kuchimba makaa ya mawe, atahitaji bilions of money kufikia hayo madini, ana hiyo mitambo? Hana. Hivyo, naomba tutengeneze Mfuko wa Wachimbaji Wadogo ambao tutau-tax kutoka kwenye mapato yetu tunayoyapata sasa hivi ili watu wajue kuna center ya kuweza kuwasaidia mahali fulani ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, swali langu, Wizara inayo mpango endelevu wa madini ndani ya nchi hii? Tuna deposit ya dhahabu, tuna deposit ya almasi, je tunajua tutakuwa nayo hii dhahabu na almasi kwa miaka mingapi? Tukiulizana leo, tusije tukaendelea kuchimba baada ya miaka 15 tukabaki tuna sifuri na mwisho wa siku hatujawa na mpango endelevu ambao unatuonyesha ni nini tunakifanya ndani ya nchi! Wizara iandae mpango endelevu unaoonyesha haya madini tuliyonayo yanaweza kwenda mpaka muda gani? Ili mashimo yaliyochimbwa kwenye maeneo yetu kwa kuwa wao ndiyo wanaosimamia mazingira ya maeneo yaliyochimbwa, yaanze kufukiwa kwa sababu yamekuwa mengi sana katika maeneo tuliyopo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niseme….

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa kengele ya pili imeshagonga.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuchangia Wizara hii ya Elimu. Kwa sababu ya muda nitachukua maneno machache ya kuchangia hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee elimu bure. Hii elimu bure ambayo tuliianza mwaka 2016 ilikuwepo siku nyuma inatupelekea mwaka 2022 kuwa na wanafunzi wengi watakaoingia sekondari. Nashukuru kwamba Wizara ya Elimu ambayo ndiyo Wizara ya kisekta ikishirikiana na TAMISEMI imekuja na mpango ambapo kutakuwa na shule 1,000 zitakazoongezwa kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukweli ni kwamba ukigawanya kwenye halmashauri zetu utaona kila halmashauri itapata karibu shule tano, kama unafanya ugawaji sawia ule. Mahitaji halisi yaliyoko kwa wananchi wetu sasa ni karibu kila kata inahitaji sekondari nyingine kutokana na wingi wa hawa wanafunzi. Kwa mazingira hayo niishauri Wizara pamoja na mpango mzuri waliokuja nao Waziri na Naibu Waziri na hata TAMISEMI wa shule 1,000, zitakuwa hazitoshi kuhimili wingi wa wanafunzi ambao tutakuwa nao baada ya elimu bure kuingia sekondari, karibu kila kata lazima iongezewe sekondari nyingine moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine ambacho nasimama kuishauri Wizara ya Elimu hapa kama nchi tatizo letu ambalo tumekuwa tunalisema hapa ni uadilifu. Uadilifu ni tatizo kubwa, je, ni mahali gani kwenye mitaala yetu tunaweza kuingiza watu wajifunze uadilifu. Kwa sababu kama nchi tatizo kubwa ni uadilifu na tumekuwa tunalisema hata hapa Bungeni, je, kwenye mitaala yetu ni mahali gani kwenye shule tulizonazo wanafunzi wetu wanaweza kuwa wanapata huu uadilifu. Nafikiri Wizara iangalie ni mahali gani tunaweza kutengeneza uadilifu wa watu wetu. Uzalendo tunaweza kuupata hata JKT na mahali pengine, je, uadilifu huu tuuingize wapi ili watu wetu wawe waadilifu na tufike safari yetu ya maendeleo tunayoenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine ambalo nataka niliseme ni kutoka kwenye Jimbo langu Busanda na hata kwa jirani zangu Mbogwe, kuna majimbo makubwa kabisa ya kata 25 hayana high school hata moja. Kata 25 kubwa au kata 30 kubwa hazina high school hata moja na mpango wa Serikali ni kuanzisha shule moja, shule moja haiwezi kuwabeba hawa wanafunzi wote hata kama wanatoka sehemu za jirani na sehemu zingine ikawa ni high school ambayo itawachukua wanafunzi. Niombe sana na niishauri Wizara kwamba kwenye maeneo tuliyonayo sasa wafikirie namna ya kuanzisha high school kwenye shule za zamani na hawa ndugu zetu wa Udhibiti Ubora waende wakaone vitu gani vinatakiwa kule badala ya kwenda tu na kuonesha mapungufu waoneshe vitu gani vinatakiwa vije Serikalini na hizo high school ziweze kuanzishwa.

Mwisho kabisa kwa sababu ya muda sasa tupo tunashughulikia maendeleo ya nchi yetu, tunapeleka umeme na maji vijijini, tunaanzisha viwanda kule vijijini, wataalamu wako wapi? Tunatakiwa kwenye majimbo yetu huu mpango uliokuwepo kwenye Wizara ya Elimu wa kuweka VETA kwenye maeneo mbalimbali hautoshi. Tunatakiwa sasa hivi kwa mahitaji tuliyonayo na ongezeko la wananchi kila jimbo liwe na VETA siyo kila wilaya. Kila Jimbo liwe na VETA kwa sababu watu wataendelea kuongezeka na mahitaji ya wataalamu yataendelea kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ya muda, naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya kuweza kuchangia bajeti na hotuba ya Waziri wa Uchukuzi. Nimpongeze sana Waziri, Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimebahatika kufika Dar- es-Salaam na miji mingine midogomidogo ambayo


inaendelea kukua Tanzania. Naomba tu niishauri Serikali nimeona pale Dar-es-Salaam tukiendelea kujenga barabara kwa ajili ya kupitisha mabasi ya mwendokasi. Nina mashaka sana kwa ongezeko la watu wale tukiendelea ku-invest kwenye mabasi yale inawezekana tusifanikiwe sana tunatakiwa twende kwenye commuter train. Tuwe na train ya umeme ambayo itakuwa inachukua watu wengi badala ya kuondoka basi moja na watu 65 au watu 30.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niishauri sana Serikali, iangalie pamoja na mipango iliyofanya katika miji yetu hii inayokua ianze kufikiria namna ya kuweka commuter trains ambazo ni za umeme ili ziweze kupeleka mabehewa
10. Tulifanya majaribio ya train pale inaitwa train ya Mwakyembe Dar-es-Salaam, ilikuwa inachukua watu wengi. Kwa hiyo, niseme wazi miji yote inayokua tuanze kwenda huko sasa tukiendelea tu kusema tutaendelea kuwa na barabara tutajikuta tunaingia carpets, carpets itakuwa constant, lakini operation cost ya kuendesha mabasi itakuwa kubwa na mwisho wa siku miradi hii itakuwa haiwezi kuizalishia nchi hii. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende kwenye barabara. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri ameonesha wazi kwamba, mpaka Aprili Serikali ilishachangia asilimia 67.2 ya bajeti ya maendeleo ambayo ilikuwa imetolewa na Serikali. Kwa hiyo, ukurasa namba tisa unatuthibitishia kwamba, Serikali imeshatoa pesa asilimia 67.2, lakini ukurasa namba 11 kwenye utekelezaji wa miradi hii kwenye asilimia 67 iliyotolewa inaonesha wazi kwamba, wametekeleza miradi iliyokamilika kwa asilimia 30 tu. Kwa hiyo, 67 ambayo imeingia imeweza kufanikiwa kufanya kazi ya asilimia 30 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mahali hapa naona kabisa kutakuwa na shida ya usimamizi. Nilitegemea ilipoingia asilimia 67.2 tuone na miradi iliyokamilika iwe hata asilimia 50, sasa ni asilimia 30 ikionesha kabisa kuna hoja ya usimamizi hapa. Kwa hiyo, nimshauri Waziri, viongozi wetu walio kule ambao wanafanya kazi kwenye Serikali wahakikishe


kwamba, kile kinachoingia kwenye Wizara kinaweza kuwa kimetumika na wananchi wakaona mafanikio yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nihamie sasa jimboni kwangu. Kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inaoneshwa wazi kwamba, kuna barabara inajengwa kutoka Geita kupita Bukoli – Bulyanhulu hadi Kahama, uchambuzi yakinifu umekwishafanyika. Niwapongeze Waheshimiwa Wabunge waliokuwa wanachangia asubuhi, walikuwa wanasema kuna uchambuzi yakinifu, kuna uchambuzi gani, kila aina ya uchambuzi umeshafanyika, lakini barabara hii bado haijajengwa na imewekewa loti tatu; kuna loti ya kwanza kilometa 54, kuna loti ya pili kilometa 61, loti ya tatu kilometa 64, lakini bado hakuna kinachokwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa sababu mvua imenyesha sana, pamoja na kwamba, iko kwenye mpango wa kujengewa lami, sasa imeharibika sana kiasi ambacho haipitiki, wananchi wanapata shida kupita pale. Niombe sana kama mipango hii ya Serikali bado iko mbali basi hii periodic maintenance ifanyike, ili wananchi waendelee kuitumia katika viwango vya kawaida wakati tukisubiri lami hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, naamini barabara hii anaifahamu na ni barabara muhimu kwenye eneo letu la kutoka Geita kuja Kahama na badaye kuja Dar-es-Salaam. ina mapato ya kutosha, tujengewe barabara hii ili wananchi wale waweze kuona matunda ya uhuru wa nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, TANROADS kwa kawaida wanatakiwa kusimamia barabara zetu nyingi kwa sababu, TARURA tumethibitisha ndani ya Bunge hili kwamba, Mfuko wao wa ujenzi wa barabara ni mdogo na bahati mbaya sana barabara nyingi ziko TARURA, za vijiji. Sasa napendekeza barabara zote ambazo zimefikia viwango vya kupandishwa hadhi kwa namna ya mgawanyo huu ambao unaendelea kuwepo kati ya TANROADS na TARURA basi zirudi kule ili zipate periodic maintenance ambayo inatambulika kwa sababu,


sasa hatutabiri tena. Mvua imenyesha barabara zote zimekatika, tukiuliza TANROADS anatengeneza? Hapana, sio ya TANROADS hii, ya TARURA hiyo kwa hiyo, haitatengenezwa msimu huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sana Serikali iangalie, tunaomba mara nyingi kupandisha barabara zetu. Kwetu kule tuliomba barabara ya kutoka Katoro kupita Rwamgasa kupita Iseli kwenda mpaka Nyarugusu ipandishwe, wanasema vigezo bado havitoshi. Tumeomba barabara ya kutoka Katoro kupitia Igondo – Nyakamwaga kwenda Kamena, wanasema ni feeder roads bado vigezo haviridhishi. Hizi barabara zinakaa hadi miaka mitano bila kutengenezwa na hivyo zinakuwa hazipitiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hilo ziko ambazo zinatengenezwa kwenye periodic maintenance. Tunazo barabara ya Chibingo kwenda Bukondo Port inatakiwa ifanyiwe periodic maintenance, haijafanyiwa, kwa hiyo, imeanza kuharibika sana na wananchi wanapata shida kupita pale. Vile vile tunayo barabara ya Mgusu kwenda port ya Nungwe kwenda ziwani nayo imeanza kuharibika bado haijafanyiwa periodic maintenance.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo pia barabara ya Katoro kwenda Ushirombo, imeanza kutengenezwa, lakini kasi yake ni ndogo. Ningeomba waongeze kasi sana ili wananchi wale sasa mvua hii inapopita barabara hizi ziendelee kupitika, kwa sababu ni feeder roads ambazo zikikatika tunashindwa kufanya zozote katika jimbo letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kama walivyosema wenzangu, kuna mipango mingi sana na watu wanasema pesa hazitoshi, lakini naamini kama Serikali imechangia tulichopanga mwaka jana asilimia 67, halafu sasa bado tunasema leo tuna mwezi mmoja bado mbele, kama itachangia asilimia 10 tutakwenda kwenye asilimia 77. 77, lazima ioneshe kitu ambacho kinaonekana kimetengezwa kwa asilimia 77, lakini utekelezaji wetu kama nilivyosema mwanzo ni asilimia 30.


Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe sana usimamizi kwa maana ya viongozi walioko kwenye wilaya zetu, walioko kwenye mikoa yetu wasimamie vizuri kuhakikisha kwamba miradi hii inakamilika. Ikiwezekana kama tutapata pesa asilimia 70 basi asilimia 70 iwe imefanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maneno haya, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nikupongeze sana kwa kuchaguliwa na kuteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bunge. Pia nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo amenipatia kuweza kuchangia Wizara hii. Wizara hii ni nyeti na yenye mambo ya kisasa nafikiri kuliko Wizara zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita kwenye mambo machache sana, kwanza ni tower sharing, co-location. Nilitegemea kabisa kwa sababu tumeingia kwenye tower sharing au co-location hiyo basi hatuna haja ya kuwa na minara mingi nchini. Kwa mfano, Kiyegeya kuna minara nane, tunategemea minara hii ipungue kwa sababu tunaweza ku- co-locate tukawa na minara miwili ikafanya kazi yote ya minara nane iliyopo na tukaokoa mazingira yetu badala ya kuwa na minara mingi ndani ya nchi ambayo haina kazi kubwa sana tuwe na minara michache na co-location iipunguze hiyo minara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tukiipunguza minara hiyo basi tutoe hizo structures huko milimani zisiendelee kuharibu mazingira tuliyonayo na hayo ma-dishes ambayo yanaonekana yatakuwa hayana kazi. Toka tumeanza kufanya co-location ni karibu miaka saba, nane, sina uhakika Wizara ina minara mingapi ambayo imei-demolish na sasa tunajua imepungua kiasi fulani na hali yetu ya mazingira kwenye milima yetu imekuwa bora, sina uhakika sana. Nishauri Serikali tupunguze idadi ya minara kwa sababu tunaweza kufanya co-location au sharing. Sharing itiliwe mkazi ili minara isiendelee kusambaa kila mahali a ku-pollute mazingira yetu, kila mtu anaonekana ana mnara wake na anataka kuwasiliana na wananchi walewale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ambalo nataka nilichangie hapa ni mkongo huu, nimesikia unaongelewa sana. Ukienda kule wilayani baada ya teknolojia kuongezeka tunatumia mifumo kulipa, mifumo mingi ya Serikali sasa inatakiwa iwalipe wakandarasi na wananchi, mkongo unapokuwa una shida maana yake ni kwamba kwenye wilaya kule kila anayeenda kufanyiwa malipo anaambiwa leo mfumo hauko vizuri, lakini shida yetu ni huu Mkongo wa Taifa. Inaonekana kabisa inter-connections imeshafanyika mahali pakubwa sana, lakini kuna udhaifu mkubwa sana kwenye maeneo ya vijijini kwa sababu ya uhakika wa hiyo bandwidth ambayo inaenda huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna maneno mazuri sana tumeyataja, lakini ukienda kwenye wilaya kabisa kule ndani ndani kule ambako ndiyo tunasema Mkongo wa Taifa umefika tumefanya hiyo inter-connection utagundua kuna wakati wanashindwa kufanya shughuli zao kwa sababu leo mtandao uko chini. Niiombe sana na niishauri Serikali ifanye ukaguzi wa kutosha kwenye maeneo hayo ili wananchi waweze kuhudumiwa na teknolojia hii kwa urahisi zaidi badala ya kuingia kwenye tatizo ambalo inaonekana malipo hayawezi kufanyika na vitu vingine vinakuwa vimesimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nirudi sasa Busanda jimboni kwangu, tuna kata 22. Kila nikikimbia kilometa mbili- tatu mtandao unapotea, maana yake coverage yetu ya mtandao ni dhaifu, hiyo radius ya coverage itakuwa ni dhaifu. Niombe sana huu Mfuko wa Mawasiliano (UCSAF) ambapo kazi kubwa nimesoma hapa kwenye hotuba hii inaonesha ni kuimarisha na kuongeza mtandao wa mawasiliano kule vijijini, vijijini mawasiliano bado yana shida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia wenzangu wanasema wanaomba hata wachangie mafuta ili Mawaziri waweze kwenda, mimi sitachangia. Niombe tu mje muangalie uhalisia kwamba kuna zaidi ya kata 11 mawasiliano yake yana matatizo. Naamini kabisa mkifika huko tuna-test wote tutajua kabisa mahali fulani hakuna mawasiliano na mtaweza kutusaidia. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nishauri sasa mizunguko yenu ifike kwenye maeneo yetu ambayo tunawakilisha wananchi waweze kupata kupata mawasiliano, wakipata mawasiliano tutakuwa na uhakika wa mambo kdhaa ambayo sasa hivi hayapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiwa kijijini leo, kwa mfano niko Kata ya Nyakagomba ambako natoka mimi, kuna walimu wanataka kufanya application nikimwambia fanya application halafu unirushie hapa, hawezi kurusha. Kwa sababu akifanya application anagundua hakuna 3G kuna 2G, kama kuna 2G maana yake kile anachofanya hakiwezi kuingia kwenye data. Kwa hiyo, tuna shida hiyo kwamba,iko minara ilikwenda vijijini kule, lakini iko kwenye 2G hawajaingia kwenye 3G na huku mbele kwenye 4G na huku tunakokwenda kwenye 5G sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana mpite kwenye maeneo ya vijijini. Namuona Ndugu yangu hapa Burongwa anagonga mkono, anajua kabisa Burongwa kule 2G ndio iko 3G hakuna. Kwa hiyo, niombe sana tutembeleeni huko tuliko ili matatizo haya ambayo tumeyata hapa tukayaseme na nyie mkiwa mnaona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina kata 13 zinachimba dhahabu. Wanachimba dhahabu, pesa wanayo, hawawezi kuwasiliana vizuri. Nilifikiri ukiwa na pesa inabidi maisha yako yawe rahisi kidogo, unakuwa na pesa lakini na maisha yako yanaendelea kuwa magumu. Niombe sana tufanyiwe huduma hii kama ni UCSAF, kama ni hawa vendors wengine waweze kuja kwenye maeneo yetu kuhakikisha kwamba tunapata mawasiliano. Tukishayapata hii kasi ya maendeleo na mchango wa sekta hii ambayo najua unaendelea kukua haraka kwenye pato la Taifa, niwaombe sana tuweze kuweka mchakato wa kutosha kuhakikisha kwamba wananchi wote wanaweza kupata mawasiliano na mwisho wa siku tutaona maendeleo yetu yanakwenda kasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu kwenye mawasiliano sasa hivi wanaweza kufanya operation, mtu akiwa South Africa anaweza kufanya operation Benjamin Mkapa akiwa kwenye mfumo huu. Sasa kama tutaonekana kwamba sisi mawasiliano yetu ni dhaifu maana yake akianza kufanya operation kuna mahali patakatika na huyu mgonjwa atafia kitandani huyu. Kwa hiyo, niombe sana tuwe na stable communication, lakini coverage yetu sasa iongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ambayo umenipatia. Lakini namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo nimeipata ya kuzungumza ndani ya Bunge hili siku ya leo katika Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nikupongeze sana kwamba vinasaba hivi vimezungumziwa sana, lakini nafikiri umekwenda kwenye conclusion kwamba sheria ije sasa ili twende kwenye maamuzi TBS wapate kihalali kutokana na sheria.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo, naomba nisijielekeze sana huko, nijielekeze kwenye umeme hapa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, kwamba katika bajeti hii, nimeona bajeti za mwaka jana na mwaka huu, wao kila wanapotenga fedha za maendeleo zinakuwa karibia asilimia 98, ikionesha kabisa kwamba kuna kazi inakwenda kufanyika. Kwa hiyo, vitabu vyao vyote vinaonesha asilimia 98 huwa inakwenda kwenye maendeleo. Na haya tunayaona kwenye miaka mitano, sasa tuna vijiji zaidi ya 9,000 vilivyoongezeka kuanzia mwaka 2015 ambavyo vimepata umeme.

Mheshimiwa Spika, mwaka huu inaonekana bajeti imeongezeka kwa asilimia nane, kwa hiyo ninaamini kazi inayokwenda kufanyika itakuwa ni kubwa kuliko hata iliyofanyika mwanzo.

Mheshimiwa Spika, niseme tu, umeme wetu huu ambao ninauona umewekwa kwenye vijiji vyetu, pamoja na miradi mingi ambayo imefunguliwa hapa katikati, bado tuna kazi kubwa ya kupeleka kwenye vitongoji vyetu, huko kwenye senta tu za vijiji na wananchi wamefurahi sasa kupata umeme, kila mmoja ambaye hana umeme sasa anajuta. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niwaombe sana Wizara wajitahidi na wakandarasi ambao wametupatia simu hawa tunaendelea kuwasiliana nao umeme uwezo kuwafikia wnanachi kwa ajili ya kuchachua maendeleo ambayo yalikuwa yamesimama kwa sababu ya kukosekana kwa umeme.

Mheshimiwa Spika, tuna vijiji 1,956 havijapata umeme, jimboni kwangu katika vijiji 83 nina vijiji 26 tu ambavyo vina umeme, vijiji 57 havijapata umeme. Kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, mkandarasi ambaye nimeongea naye jana – nilipata namba yake – ameniambia bado anashughulikia performance bond CRDB, kwa hiyo, bado hajaweza kwenda kwenye eneo la tukio kwa ajili ya kutupatia umeme.

Mheshimiwa Spika, niwaombe sana; katika miaka miwili ambayo tumeambiwa Desemba, 2022 kutakuwa na umeme nchi nzima, tuhakikishe kwamba umeme huu unaosemwa uweze kufika kwenye vitongoji ili wananchi waweze kuona maendeleo ambayo tunayasema.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo moja, nimeona wanasema kuna densification. Hii densification kuna mahali ambapo watu wameshafanya wiring muda mrefu tu, lakini walivyokuwa wanafanyiwa survey maelezo yanasema kunatakiwa nguzo mbili, hawezi kuwekewa umeme ule, anatakiwa tena aingie kwenye hii densification kwa sababu anaonekana yeye hapo alipo siyo kijiji, ni sehemu tu ya mtaa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, yako maeneo mengi ambayo yanakaribiana na miji midogo hii yana tatizo hili; watu wengi wamefanya wiring na hawana umeme, na malalamiko yao ni makubwa. Ninaomba sana Mheshimiwa Waziri, hawa wakandarasi wanaokwenda, pamoja na miradi hii ambayo tumeisema, uweze kuwasaidia wananchi hawa waweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye umeme hapo; pamoja na kujenga miundombinu ambayo tunaisema, kuna tatizo kila ninapokwenda ninalikuta mahali kwenye miji yetu. Umeme unapowekwa kati ya nguzo na nguzo kuna kitu wanaita clearance, clearance ni mahali ambapo nikisimama natakiwa nione wire ukiwa juu yangu. Lakini bahati mbaya kwenye miji yetu hii unaweza ukasimama ukaona wire umepita tu karibu nusu mita kutoka kwako ulipo.

Mheshimiwa Spika, sasa huu ujenzi wa miundombinu ya aina hiyo udhibitiwe sana kwa sababu wanaita mawimbi (magnetic feed), yale mawimbi yanapopita karibu na mwanadamu yana athari, na hizo athari inawezekana zisitokee kesho au keshokutwa, zikaja baada ya muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunapojenga laini zetu hizi tuhakikishe kwamba ile clearance ya mwnadamu kwenda kwenye wire iwe ni ile iliyokuwa-recommended, iliyosemwa. Ukienda kwenye miji mbalimbali unapita unakuta wire unapita tu jirani, maana yake ni kwamba ujenzi uliofanyika ulikuwa chini ya kiwango.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niishauri Serikali kwamba ujenzi wa laini zinazojengwa wahakikishe kwamba hicho kinachojengwa kama clearance kwenye ile sag kati ya nguzo na nguzo kiwe ni kile ambacho kiko recommended kwa ajili ya mwanadamu ili mawimbi yale, magnetic feed, isimletee madhara kwa namna yoyote ile. Kuna mahali inaoneshwa hata kwenye mitandao mtu anapita karibu anagusa wire. Ni hatari sana kwa maisha yetu.

Mheshimiwa Spika, nihame kwenye umeme niende kwenye EACOP (Bomba la Mafuta). Hili bomba la mafuta limesemwa muda mrefu na wananchi wetu wamekuwa wanajiandaa wanajua watauza mchicha, mayai na kuku. Lakini hivi vitu kama alivyosema jirani yangu hapa, Mheshimiwa Zedi, havijana defined. Havijajulikana ni vitu gani vitafanyika kwenye biashara ya bomba la mafuta, sasa vingesemwa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niishauri Serikali kupitia Taasisi ya Uwezeshaji, kwamba ingewezekana wananchi ambao tunao wako wengi wanaotaka kufanya biashara kwenye bomba la mafuta lakini uwezo wao ni mdogo. Hii Taasisi ya Uwezeshaji ambayo ninaamini ipo katika Ofisi ya Waziri Mkuu, waangalie uwezekano wa kuwa na fedha ambayo itapitishwa kwenye benki yoyote ili iweze kuwasaidia hawa wafanyabiashara wadogo na wakiweza kukopeshwa kwa utaratibu wa benki wataweza kufanya biashara hizo. Ili isifike biashara hii ikavamiwa na wageni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusipofanya hivyo wako watu wamejiandaa kufanya biashara na bomba la mafuta, wataonekana kama ni Watanzania lakini itakuwa ni hela kutoka kwa watu wengine wenye uwezo mkubwa na siyo wale Watanzania wenyewe. Kwa hiyo, hii Taasisi ya Uwezeshaji iangalie inaweza kupita mahali gani kwenye benki zetu ikawawezesha hawa waweze kufanya kazi katika miaka hii.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu mtu atahitaji labda kuku 1,000, tukiuliza kuku 1,000 nani anao ili aweze ku-supply, utaona mwananchi anaanza kuhangaika, anakusanya huku na huku. Lakini kama wamewezeshwa watakuwa wameandaliwa kwa ajili ya kuvuna hiki ambacho tunakisema ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikumbushe suala la mwisho kwa Mheshimiwa Waziri; kuna mradi kutoka Geita, Mpomvu kwenda Nyakanazi, ambao ndugu yangu, Mheshimiwa Ezra, aliusema pale. Huu mradi umesemwa muda mrefu sana lakini haukamiliki. Kwa hiyo, ni ombi langu Mheshimiwa Waziri, hawa wakandarasi wanaokuja sasa wahakikishe kwamba mradi huu unakamilika, vijiji vingi sana vinapitiwa na mradi ule na kama haukamiliki maana yake wale wananchi hawawezi kupata umeme kwa sababu ndiyo laini pekee kwenye backborn inayoweza kuwapelekea umeme.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ENG. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii niliyopatiwa ya kuzungumza leo lakini nakushukuru sana Mwenyekiti kwa nafasi vile vile ambayo umenipatia kuweza kuchangia kwenye mapendekezo ya mpango huu wa mwaka mmoja 2022/2023. Binafsi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa Kazi kubwa anayoifanya na kwa mambo mengi ambayo ameyatoa ikiwemo bajeti ambazo zimekwenda kwenye majimbo yetu matokeo tunayaona tunaamini kwamba kazi inayoendelea kufanya ni nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa kutuletea mpango huu mpango ambao tumeupitia na kuusoma unatupeleka mahali fulani kwenye maendeleo tunayoyatarajia, lakini nimpongeze Mwenyekiti wa Kamati ambaye naye alishauri mambo mengi katika hotuba yake ikiwemo sehemu kubwa ambayo nitachangia ya Kilimo. Binafsi ni muhumini wa Kilimo leo na ninaona kilimo bado kuna kazi kubwa ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kilimo mwaka jana ilitolewa fedha ya bajeti kama bilioni mia mbili na kitu hivi ambayo kwenye hesabu bilioni mia mbili kati ya tirioni karibu 33 ni fedha kidogo haifiki hata asilimia moja na bado nimeona michango mengi mwenyekiti wa kamati anapendekeza ikiwezekana wapewe bilioni mia nne inaweza ikaleta mchango fulani kwenye maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siamini kwamba kutoka uhuru sasa tunaingia miaka 60 hivi karibuni baada ya mwezi mmoja tutakuwa tunasherekea miaka 60. Tumekuwa na slogans nyingi Kilimo kwanza, uhuru yaani yako maneno mengi ambayo tumeyasema lakini bado Kilimo hiki kinaonekana hakiendi maana yake ni kwamba hatujaamua kufanya kudhamiria kuingia kufanya kazi kubwa kwenye kilimo hiki. Nami nimependekeze tu kwanza hata kabla sijasema kwamba ni vizuri kabisa kwenye bajeti yetu asilimia kumi ishughulike na kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana bahati nzuri ni mhandisi hatuwezi kupanda mlima kwa gear namba tatu lazima tuondoe namba 1 ikiwezekana mahali fulani tuweke hata hiyo gear ndogo ili tuweze kupanda vizuri sasa tumekuwa tukienda tunakwenda kwa mwendo wa pole pole ambao ninaamini hauwezi kututoa. Kwa mfano, tuna hekta ambazo zinafaa kwa umwangiliaji milioni 29.4 sisi kama nchi tuna scheme ambazo zime-cover 0.4 milioni hekta yaani hatujafika hata milioni moja kwenye zile 29 na bado tunajinasibu kwamba watu asilimia zaidi ya 66 wameajiriwa kwenye sekta hii ya Kilimo hatuwezi kufanya kitu, hizi sekta za uzalishaji lazima zipewe fedha za kutosha tudhamirie kufanya hiki kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesikia wenzangu wanachangia wanaogopa hata kukopa na nini, kukopa hatuna haja ya kukopa bado deni letu stahimilivu hatuna haya ya kuogopa kukopa, tukope tuingie kufanya kazi hii ya kilimo ionekane. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo kadhaa ambayo nafikiri tunatakiwa kuyafanya kwa mfano; tunatakiwa kuhakikisha kwamba tunaporesha hafua za mifugo Kilimo na Uvuvi ambazo ni sekta za uzaliishaji lazima ziboreshwe, lakini tunatakiwa tuboreshe hafua zinazo husika na upatikanaji wa vyakula lakini malisho vile vile na maji, tunatakiwa tuboreshe hafua za huduma za afya za mimea, mifugo na viumbe maji, lakini tunatakiwa tuboreshe hafua za huduma za ugani na usafiri na mafunzo kwa hawa watu wanaoenda kushughulika na kilimo, tunatakiwa tuboreshe hafua za usindikaji na masoko kwa maana na masoko na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vile vile, tunatakiwa tushughulike kuhakikisha kwamba tunaporesha M and E Monitoring and evaluation ufuatiliaji wa hii miradi. Sasa siku zote tumekuwa tunazungumza tunataka tuweke milioni mia nne je, ukifikiria sekta ya maziwa peke yake mpaka leo ninavyozunguza hakuna tone la maziwa nchi hii zinazouzwa nje ya nchi hata lita moja haiuzi, lakini ndani ya nchi bado yako maziwa yanamwagwa huko maporini kwenye maeneo tunayotoka kwa sababu gani hakuna mahali pa kwenda kuyatunza yale maziwa hayawezi kukaa siku nne wala siku tano na sisi tunasema tutaweka bilioni mia nne mwaka jana tuliweka bilioni 200.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mpango huu ukifungua mapendekezo ukurasa namba 63 utagundua tulivyokwenda kwenye kilimo tumepima sample 1,858 kwenye nchi nzima unaweza kupima sample 1,858 za udongo halafu unataka kulima utafiti gani huu tunaufanya siyo kwamba wataalam hatuna namna ya kuwawezesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nafikiria nisiseme maneno mengi sana tukubali kwamba sasa Serikali inakwenda kukopa fedha na kuingiza kwenye Kilimo Mifugo na Uvuvi. Niwapongeze Serikali wanaonyesha kabisa kwenye ukurasa namba 18 kwenye kipengele namba 15 ambacho ni XXV kwamba kwenye fedha za covid 19 wamekwenda kuweka bilioni 5 kwenda kusaidia wajasiliamali wadogo wadogo kuboresha vibanda vyao sijui kama itakuwa imeonekana vizuri hii, watu wanaona kama wajasiliamali wadogo wameguswa kwenye hii hotuba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hapo napo nataka iongezwe kwa sababu wajasiriamali hawa wadogo ndio wakulima wetu, ndio wanaofanya shughuli zote huko tuliko iwekwe fedha bili uoga ukidhamiria kumsomesha mwanao ukaanza kuogopa kila siku hata maliza shule ndiya sababu tumekuwa na miaka 60 lakini bado sekta hizi ambazo zinatakiwa ziwezeshwe ili uchumi uchangamke bado hauchangamki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi wote ni mashahidi kwamba pato la Taifa linachangiwa kwa asilimia 26.4 na Kilimo. Sasa tunaogopa nini yaani unajua kabisa kwamba huyu ndiye anayeleta maziwa mengi kwanini usimlishe majani ya kutosha ili atowe maziwa mengi wasiwasi wetu ni nini kama Serikali. Hatuna haja ya kuogopa tuingize fedha kwa sababu hii ni production sector tunaamini kabisa fedha ile itarudi kwa sababu hii itakuwa kama biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme wazi kwamba hoja yangu ya leo nataka nijikite hapa tunaanzisha vikundi vidogo vidogo huko tulipo vya wakulima, vikundi vidogo vidogo vya wavuvi, vikundi vidogo vya wasindikaji. Niseme taarifa njema leo nilikuwa kwenye tamasha la wine pale ni NMB wamesema wasindikaji wale processors wote wanakopa kwa asilimia 10 tu humu nasikia wanasema riba itakuwa asilimia 30 wasindikaji imeshatolewa wanakopa kwa asilimia 10 tu. Kwa hiyo tunauwezo wa kufanya usindikaji processing ya kwetu kwa asilimia 10 hiyo. Kwa nini tunakuwa na mashaka, Serikali ikope tuingie huko tufanye hivi vitu. Maziwa yakatunzwe, maziwa yakasindikwe, maziwa yakawe processed tuanze kufanya biashara na soko la nje. Nina amini kabisa tukichangamsha hizi sector za uzalishaji uchumi wetu utaamka na utakuwa mkubwa kuliko ulivyo leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru kwa kunipatia nafasi hii. Vilevile namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya kuchangia katika Mapendekezo ya Mpango wa Taifa wa Mwaka 2023/2024. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kutuletea Mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekit, kwa kuanza kabisa, kwa sababu Dira ya Taifa ya 2025 inaenda kwisha nilitegemea nione kuna mahali panaonesha kwamba sasa tunaanza Dira ya Taifa nyingine mpya ambayo wengine wanaiita ya muda mrefu, wengine sijui wanaita nini; kama ni ya miaka 50 ndiyo tutafanya break down ya namna gani tutafanya kazi. Hii ishirikishe wananchi na wadau mbalimbali ili kusudi tuwe na dira ambayo itakuwa ni shirikishi. Kwa hiyo, naomba sana kwenye Mpango huu nione mahali ambapo kwenye bajeti zetu tunaingiza hiki kitu kwasababu tumebakiza nafikiri mipango miwili na hii itakuwa inakwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda ukurasa wa nne wa Mpango wa Mapendekezo tuliyoletewa hapa, utagundua kuna takwimu za ukuaji wa uchumi katika Mataifa yetu haya kwa maana ya East Africa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukienda ukurasa wa nne wa Mpango wa Mapendekezo tuliyoletewa hapa utagundua kuna Takwimu za Ukuaji wa Uchumi katika mataifa yetu haya kwa maana ya East Africa. Kumbukumbu zangu ambazo nimezitoa hapo zinanionesha Kenya mwaka 2019 uchumi wao ulikuwa unakua mpaka 4.9, mwaka 2020 ikaenda negative 0.3, mwaka 2021 wameenda 7.2, maana yake waemsukuma kwa nguvu 7.2 unaongeza na 0.3 wameenda 7.5. Nchi ya Rwanda walikuwa 9.5 ilivyofika 2020 wakaenda negative 3.4, lakini 2021 wakaenda 10.2. Ukienda Sudani walikuwa 0.9 wakaenda mpaka negative 6.6 kwa sababu ya corona, lakini wamekwishajivuta wamekwenda mpaka 5.3.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tulikuwa 7.0 hatukwenda kwenye negative tulikwenda mpaka 4.8 na tumejivuta tuko 4.9 maana yake tumeongeza 0.1. Uganda walikuwa na 7.2 wakaenda mpaka negative 1.4, sasa wamefikia 5.1 maana yake wamekwishakwenda kama 6.5. Burundi walikuwa 0.8 wakashuka mpaka 0.3 sasa hivi wemekwenda 2.4 maana yake wameenda 2.7. Sisi tunakua kwa 0.1 mpaka 0.4 maana yake kuna tatizo hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuunge mkono ndugu yangu jirani yangu hapa Mheshimiwa Mwijage anaposema tuwe na Tume ya Mipango. Jana Mheshimiwa Ndugulile alisema Tume ya Mipango, maana yake hatujagusa mahali ambapo uchumi wetu unaweza kuchangamka, tunagusa, lakini tunagusa kwa kukua kwa 0.1, maana yake data haziwezi kudanganya ukuaji wetu ni mdogo kulinganisha nan chi zote za East Africa. Maana yake tunachokifanya sisi hatujagusa mahali pake. Ni wapi hatujagusa, ni kwa sababu hatujaingiza pesa ya kutosha kwenye productive sectors. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuwezi kuwa na majibu rahisi kwenye maswali magumu. Tunatakiwa kwenda na wenzetu kwa sababu tunaenda kwenye mikutano, tunazungumza nini wakati wao wamekuza kwa 7.5 sisi tumekua kwa 0.5 au 0.4? Maana yake sisi tunavutwa badala ya kuendelea kutembea na wenzetu, sisi tunavutwa nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika robo ya kwanza ukuaji wetu wa pato la Taifa unaonekana umekwenda kwenye 5.2, maana yake tuna-predict kwenda kwenye 5.3 ndio maoteo yanavyoonesha. Kwa hiyo, hata malengo yetu ya ukuaji ni madogo, yaani ukijiwekea malengo madogo unategemea process yako nayo itakwenda kwenye malengo madogo. Kwa mfano, tunategemea kuona Ziwa Viktoria linashughulikiwa kufanya umwagiliaji wa kilimo chetu. Sijaona mahali popote tumeanza kumwagilia kwa Ziwa Viktoria. Tunasema tu mvua hainyeshi, kule maji yapo, kwa nini tusianzishe skimu ambazo zinatoa maji Ziwa Viktoria, zinatoa Nyasa, zinatoa Lake Tanganyika badala ya kuanza kushughulika na maji ambayo ni non predictable? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu wazi Mpango huu naomba uangaliwe vizuri tunapoenda kwenye utekelezaji wake, lakini Mpango huu umekuwa mara nyingi Mipango yetu ya Miaka Mitano, hoja yetu kubwa ilikuwa ni kuchochea uchumi shirikishi na shindani. Tuna miradi mingi sana tumeisema, iko mingi sana ambayo imefanyika ya barabara na niseme tu wazi kama kuna mahali ambapo pamoja na mambo tuliyoyafanya mwaka jana na bajeti yetu bado ile ahadi ya kuongeza mtandao wa umeme kwenye vijiji vyetu ya kilometa mbili haijafanyika. Kwa hiyo, uwezo wa wananchi wetu ku- access umeme bado ni kilometa moja ile ya kwanza, tuwaongezee hizo kilometa mbili ili uchumi huu uweze kuchangamka, bila hivyo hauwezi kuchangamka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile vijiji ambavyo tuliona bado havina umeme vipate umeme. Yako mambo mengi ambayo yameandikwa kwenye ripoti yako kwenye page number 21 na TEHAMA. Watu wamekuwa wanazungumza hapa, inaonekana kilimo wanasema neno lao, tunataka Wizara hizi zisomane, zi-communicate. Kwa mfano, unachimba bwawa la maji, bwawa la maji tunategemea mtu wa kilimo atafanyia irrigation, wananchi watakunywa maji, lakini mifugo watawekewa sehemu zao za kunywea maji. Utakuta Wizara ya Mifugo inashughulikia bwawa lake, Wizara ya Kilimo bwawa lake, there is no communication, hawa watu wa-communicate ili matumizi ya Serikali yaende chini. Nategemea haya mambo niyaone kwenye hiyo nani hii iliyoletwa hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kulikuwa na moja, kuimarisha uwezo wa uzalishaji viwandani na utoaji wa huduma, hapa ndio kuna changamoto. Natoka kanda ya ziwa, naomba niseme ukweli, tulikuwa na ginnery 11 kule NCU, hakuna hata moja inayofanya kazi. Unategemea tunaposema tunataka tuuze processed goods kutoka kwa hawa watu ambao viwanda vyote 11viko chini watafanya nini? Kwa hiyo, kuna kitu cha kufanya hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati nzuri niseme tu kama story, nilipita juzi mahali fulani kwenye ginnery nikakuta usiku saa 4.00 wanafanya harusi, yaani sehemu ambayo walikuwa wanazalishia pamba, kuna harusi na watu wanastarehe, yaani inaonekana kabisa tumekwishatoka kwenye reli tuko mahali pengine. Turudi kwenye reli sasa kwamba, at least huko tunakotoka kwenye ginnery 11 angalau ginnery tatu zifanye kazi, tuwe na mambo ambayo sasa yanaonekana tunaweza kujenga uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kengele ya kwanza nimeisikia imelia, niseme wazi kwenye production sector. Wenzetu Waganda, nilikuwa namsikia ndugu yangu hapa, hata uki- surf kwenye internet utagundua kwamba, wao kwenye diary export yao wana dola kama milioni 220 ambayo ni milioni 500 wana-export kwa mwaka mmoja, sisi tuna-export zero na tunataka tuchangamshe uchumi. Wale ambao wanajua nilikuwa natembea juzi nafanya mazoezi, ofisi ya watu wa maziwa Tanzania iko pale kama unaenda stendi ya hapa Dodoma hapa, ukifika tu unajua hapa hamna kitu hapa, ukiiona tu ofisi unajua hamna kitu hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme wazi kuna kitu cha kufanya. Lazima tukubali tunakwenda ku-invest ili tupate kitu fulani kwa sababu, wenzetu kama wanauza bilioni 500, sisi tunauza sifuri halafu tunategemea huu uchumi wetu utakua haraka, haitawezekana. Kwa hiyo, niwaombe sana kwenye mipango hii sasa tujue kabisa tunekwenda kufanya nini kwenye productive sector na ionekane na haya tukayatekeleze, tutaona uchumi huu ukiwa umechangamka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, anasema kuna kuimarisha mifumo ya upatikanaji kwenye kilimo na sasa wanasema kule kwamba, kuna guarantee scheme ya wakulima wadogo, mimi sina uhakika, labda ninakotoka Wabunge wenzangu wanaweza kusema; wanasema wameandaa guarantee scheme, yaani skimu inayoshughulika na wakopaji wadogo kwa ajili ya kilimo, sijaiona hii, lakini kwenye mpango huu naiona imeandikwa kwamba, inaonekana kuna mpango huo. Kwa hiyo, haya mambo mengi mazuri yaliyoandikwa yawe implemented…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii. Vile vile namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi ambayo amenipatia leo kuweza kuzungumza ndani ya Bunge hili tena. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hoja yangu kubwa ni kujikita kwenye Elimu ya Msingi, lakini napenda kwanza nimpongeze Mheshimiwa Rais kupitia Waziri wa TAMISEMI na Manaibu Waziri wawili, wataalam ambao tumejumuika pamoja nao hapa kwa kazi kubwa ambayo wanafanya.

Mheshimiwa Spika, nimepitia hotuba hii, ni dhahiri kwamba katika ukurasa namba 12 na 13 ni lazima tumpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa aliyoifanya kwa kutupatia fedha katika Mpango wa Maendeo kwa ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO 19. Jimbo letu la Busanda lilipata takribani madarasa 209 ambayo yana thamani ya shilingi bilioni 4.2. Kwa hiyo, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kupitia Wizara hii kwamba tuna madarasa ya kutosha Sekondari na sasa wanafunzi wanaendelea kusoma. Vile vile nampongeza Mheshimiwa Rais kupitia Wizara hii, ametupatia fedha kupitia TARURA zaidi ya shilingi bilioni 2.2 kwa ajili ya barabara. (Mkofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niseme wazi kwamba Wizara hii inafanya kazi kubwa na nimeona kwenye mpango kwamba fedha mwaka huu imeongezwa. Ninaamini barabara zitaendelea kujengwa vizuri kuliko ilivyofanyika mwanzo, lakini niombe sasa tuna miji yetu midogo, kwa mfano, Mji wa Katoro barabara zake nyingi hazipitiki. Naomba TARURA walichukue hili na Manaibu Waziri wote wawili wamekuja Katoro, Mawaziri amepita Katoro, ameona hali halisi iliyopo, kwamba mji ule haupitiki. Tuna shilingi 600,000,000/= ambayo ilikuwepo kutoka ardhi mji unaanza kupangwa. Tunaomba ujengwe na barabara zake zipitike ili mji uweze kuonekana ni mji mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukurasa namba 15 wa hotuba ya Mheshimiwa Waziri unaonesha wazi kwamba kuna vituo vya afya 304 ambavyo vimejengwa na vinaendelea kujengwa, lakini 234 vinatokana na tozo. Tulipendekeza mwaka 2021, vituo vya kimkakati kutoka kwenye Kata zetu, mimi binafsi kwa maana ya Busanda nilipendekeza Rwamgasa, Nyakagomba na Magenge, lakini sijaviona kama vimejengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na pongezi kubwa ya kazi kubwa ambayo mnafanya, vituo hivi vya kimkakati viangaliwe kwenye maeneo yetu kutokana na jiografia. Jimbo letu la Busanda ni kubwa, nategemea kwamba mkitupatia vituo vya afya ambavyo tumevisema tutakuwa kwenye mazingira ya kuweza kuhudumia wananchi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu elimu ya msingi ambayo nilisema nataka niizungumzie, mahali popote ambapo msingi unakuwa na mashaka, ni lazima ujenzi kwenda juu, nyumba hiyo itakuwa inayumba. Elimu ya msingi ndani ya nchi hii ambayo ninaamini kwamba inasimamiwa na Wizara hii ina changamoto nyingi.

Mheshimiwa Spika, miundombinu ya elimu ya msingi Tanzania, ukipita kwenye shule za msingi utagundua mambo yafuatayo: wanafunzi ni wengi lakini madarasa ni machache. Hotuba hii inatuonesha wazi kwamba mwaka 2021 tulipanga kudahili wanafunzi kama 1,272,513 lakini tulidahili zaidi ya hapo na mwaka uliofuata ambao ni mwaka huu, tumedaili zaidi tuna asilimia 103; shule za msingi mwaka 2021 tulidahili vile vile zaidi ya asilimia102, mwaka huu tumedahili kwa asilimia 108. Maana yake hata malengo tunayoyaweka, tunazidi, wanafunzi ni wengi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye shule zetu za msingi ambazo tunategemea ziwe zimeandaliwa vizuri sana, kwa sababu kama hazijaandaliwa vizuri, hao walimu wanaokuja Sekondari watakuwa na kazi kubwa sana ya kushughulika na hao wanafunzi, kwa sababu wanatoka wakiwa hawana msingi wa kutosha. Kwa mfano, Jimboni kwangu kuna shule inaitwa Bwawani, ina wanafunzi 3,100 lakini ina vyumba vya madarasa sita. Sasa ukijiuliza, tunataka kuendesha shule, tunaiendeshaje shule hii? Kwamba tuna wanafunzi 301, lakini madarasa yapo sita.

Mheshimiwa Spika, tuna shule nyingine inaitwa Ibwezamagigo, ina wanafunzi 3,111, nayo ina madarasa sita. Tuna shule nyingine inaitwa Mchongomani, ina madarasa tisa lakini ina wanafunzi 3,319. Ukifikiria tu unaweza ukajua kama hapo ndipo tunapotaka kuwaandaa wanafunzi kwa maana ya msingi; tutakuwa tuna changamoto kubwa. Tutawachukua wanafunzi wengi watakaoenda kwenye Kidato cha Kwanza lakini watakuwa wana kasoro nyingi kwa sababu ya uhalisia huu ambao unaonekana huku chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa ni ombi langu kwa maana ya nchi hii, huu ni mfano mdogo tu; ina maana tukiwauliza Wabunge wengi hapa kwenye maeneo yao, watagundua kabisa hakuna madawati ya kutosha, tutagundua kwamba hakuna vyumba vya madarasa vya kutosha. Hii elimu ya msingi sasa Serikali ijikite hapa, kama ilivyofanya kazi kwa Sekondari, iende sasa elimu ya msingi kuhakikisha kwamba tunaweza kuboresha, kwa sababu pamoja na madarasa kuwa machache, lakini hata walimu huko kwenye shule za msingi nao bado hawatoshi. Pamoja na kwamba tunaona sasa hivi imetangaziwa walimu wanatakiwa kuongezeka, lakini walimu hata wakiongezeka bado walimu watakuwa hawatoshi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali, kama kuna kitu sasa tunatakiwa kufanya, tujitahidi sana kuboresha elimu ya msingi ili msingi ukiwa bora, watoto wetu wanaokwenda juu, waende wakiwa na msingi ulio bora. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa leo niishie hapa. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Madini. Namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ya leo aliyonipatia ya kuzungumzia Madini, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake nzima wakiwepo wataalam kwa kazi kubwa wanayoifanya.

Mheshimiwa Spika, tunaona kabisa kwamba mchango wa sekta hii sasa kutoka asilimia 6.3 katika kipindi kama hiki tumekwenda kwenye asilimia saba inaonesha kwamba lengo la Serikali ambalo lilikuwa kwenye mpango mzima kwamba mwaka 2025 tuwe na asilimia 10 linaweza likafikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwasababu lengo ni hilo na inaonekana kasi ni kubwa ningeomba sasa tuzidishe sasa tuizidi hiyo asilimia 10 ili ionekane kabisa kwamba tumefanya kazi nzuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi nitoe ushauri wa Serikali kama mchangiaji Profesa Muhongo alivyosema dunia sasa ipo kwenye energy transition, hapa kwenye energy transition maana yake tunakwenda kwenye yale madini mkakati, critical minerals na dunia ya sasa inakwenda huko. Kwa hiyo, niwaombe sana GST ambao ninaona hapa wamepewa fedha kama Shilingi Milioni Mia Moja Arobaini na Tatu tu, tuangalie namna gani tunaweza tukawaongezea ili waweze kuingia kwenye kutafiti hayo madini ambayo dunia ya sasa inakwenda.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa ninaangalia hapa Canada wana madini mengi ambayo sitaki niyataje, ni karibu 34 yanaonekana hapa kwenye hizo critical minerals, kwa hiyo niwaombe sana GST na Wizara kwa ujumla iwasaidie sana GST ili waweze kupita kwenye utafiti huu.

Mheshimiwa Spika, niliona imetajwa kidogo kwenye madini ya mkakati, lakini bado haitoshi kwasababu dunia inakwenda huko. Kama tulivyosikia China wanataka kutoa magari nilikuwa ninaona Research moja inaonesha kabisa kwamba gari la umeme linaweza kutumia kama kilo 200 hivi, lakini gari ambalo litakwenda kutumia hizi critical minerals zitatumia kama kilo 40, niliona mtu mmoja amefanya reseach kama hiyo. Kwa hiyo, ningeomba sana tuwaelekeze hawa GST wafanye utafiti wa kutosha ili dunia inapokwenda kubadilika na sisi tubadilike pamoja nao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nijikite sasa kumpongeza Waziri kwa leseni za wachimbaji wadogo 4,490 ambazo zinaonekana kwenye hotuba yake. Hizi hata kwenye Jimbo langu la Busanda kuna watu wamefaidika na leseni hizi lakini niishauri Serikali katika kuwasaidia wachimbaji wadogo nimeona kabisa inaonesha STAMICO wamepitia vikundi vitano, vikundi vitano ndani ya nchi hii kama ndiyo vinaenda kutathminiwa maeneo yao kuonekana kuna madini kiasi gani ni vichache sana, iwezeshwe STAMICO kuhakikisha kwamba inaweza kupitia vikundi vingi.

Mheshimiwa Spika, hapa vinaonekana kwenye Randama Ukurasa Na. 11, vikundi vitano tu vimepitiwa, navyo vinaonekana vimepita Kilindi, Morogoro na Singida, kule kwangu Busanda ina maana hawakupita kipindi chote hiki na kuna wachimbaji wadogo wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nijielekeze kuonesha kwamba katika wachimbaji wadogo tunaowazungumzia hawa wamekuwa wanasuasua katika kutambua mchanga au mawe kwamba yana dhahabu kiasi gani, na wamekuwa wanatumia maabara hizi za watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri mamlaka inayosimamia maabara hizi, watu wetu wamekuwa wanakwenda kupima PPM kiwango cha dhahabu kwenye udongo au kwenye mawe wanaambiwa hapa kunaonekana kuna 18 kumbe amedanganywa, anachukua mtaji mzima kuendelea kufanya kazi kwenye eneo hilo Milioni Mia Tatu, Milioni Mia Nne, akienda kusafisha chenjua anakuta Shilingi Themanini matokeo yake anapata hasara ambayo kwa kawaida inaweza kumpotezea maisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mamlaka inayohusika na maabara hizi ihakikishe kwamba inazipitia kuzikagua ili wananchi wetu wahakikishe kwamba wanapata faida badala ya kupata hasara kwa sababu wamedanganywa na matokeo yaliyofanyika kwenye maabara hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme wazi kwamba yapo maeneo mengi ambayo yameendelea kumilikiwa na watu, hawa watu wenyewe ukiwatafuta kwenye maeneo yetu wanaonekana siyo wakazi wa maeneo hayo kwa sababu ni haki yao kupata maeneo hayo lakini wananchi wetu wanahitaji kuchimba. Ninaomba maeneo hayo ambayo sasa yanamilikiwa na hayafanyiwi kazi Wizara iyashughulikie kuhakikisha kwamba yanaweza kutaifishwa yakarudishwa mikononi mwa wananchi ili waendelee kufanya uchimbaji mdogo mdogo kwa sababu asilimia 35 ya wachimbaji wetu ni wachimbaji wadogo, nao wanachangia pato hilo la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe angalizo kwamba tunaweza tukaiona Wizara hii inachangia sana kwasababu bei ya dhahabu imepanda, niwaombe sana Wizara tuhakikishe kwamba majadiliano negation teams zifanye kazi kwa haraka kuongeza watu wanaoendelea kuwekeza kwenye sekta hii. Kwa mfano, tuna special mining license mbili tu, ukiziona zimekuja mbili zimekuja kipindi hiki lakini za kwanza ambazo special mining license tumekuwa nazo zimepatikana nafikiri mwaka 2000, 2002 na 2003 kwa hiyo tuna miaka karibu 15 hadi 20 ambayo tulikuwa hatujatoa leseni za hivi karibuni.(Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa Kengele imeshagonga.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, vilevile namshukuru sana Mwenyezi Mungu kutujalia tena leo kukutana hapa na kutupa nafasi ya kuweza kuzungumza hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya ndani ya nchi hii, vilevile kazi kubwa ambayo wananchi wa busanda wanaiona inaendelea kwenye maeneo yetu. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hilo, pia nampongeza Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, manaibu wake wawili, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi nijikite kwenye maeneo matatu, kwanza Elimu ya Shule ya Msingi ambayo hata mwaka jana niliizungumzia. Tumeingia kama Taifa kwenye mmomonyoko wa maadili ambao kila mmoja sasa hivi anapiga kelele sitaki nirudie tena, lakini mahali fulani kwa sababu misingi yetu haikuwa imara ndiyo sababu tuna mashaka na kile kinachoendelea.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuna kazi kubwa ya kutengeneza msingi ili huu msingi ukiwepo basi tusipate kuyumbayumba kama kuna vitu vinaingia vipya na hapa lazima tunaanza kwenye familia zetu ambako siyo Wizara hii lakini tunakwenda kwenye Shule za Msingi ambako tunapeleka watoto wetu.

Mheshimiwa Spika, Wabunge wote watakuwa ni mashahidi kwamba Shule za Msingi nyingi zimechakaa na uchakavu wake TAMISEMI kwa ubunifu wamekuja na miradi mingi BOOST, LANES, SRWSS kuhakikisha kwamba tunaweza kuboresha shule za msingi, lakini kiukweli uchakavu ni mkubwa sana na pesa inayokwenda hiyo ni kidogo kurudisha Shule za Msingi kwenye hali yake ya kawaida. Hivi watakuwa na kumbukumbu nzuri tu kwamba hata mdororo ile drop out itakuwa ni kubwa. Watoto wengi sasa hawako- interested sana kwenda kwa sababu wanajua mazingira ya nyumbani yanaweza kuwa ni mazuri kuliko Shule ya Msingi anayokwenda.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tunategemea sasa waongeze pesa kuhakikisha kwamba shule za msingi zimeboreshwa na zikiboreshwa kama ilivyo sekondari, bahati nzuri ni kwamba sekondari zimeboreshwa, baada ya kuboresha sekondari sasa ni rahisi kujua kwamba Shule ya Msingi hii siyo bora kwa sababu sekondari ina vioo na Shule ya Msingi inaonekana wazi kwamba hii siyo bora, kwa hiyo kuna kazi kubwa ya kufanya ya kuboresha shule za msingi na tujenge msingi kwa kuweka content ambazo watoto wetu hawatayumba kama maadili yatakuwa yameyumbishwa na dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama wasemaji wa kwanza walivyosema juu ya shule za msingi, tuna maboma mengi yaliyojengwa na wananchi kwa nguvu za wananchi yanatakiwa kumaliziwa haya. Ni changamoto kubwa inapokuja kujenga madarasa mapya wakati kuna madarasa hayajaezekwa yako matano shuleni pale. Wananchi wanajiuliza hawa wameona nini waje wajenge mapya haya ya kwetu wayaache? Kwa hiyo, ni ombi langu TAMISEMI waangalie uwezekano wa kuyamalizia hayo maboma ambayo yamekwisha anzishwa na wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo yangu kwa uchakavu huu tu nina mifano michache, nina shule kwa mfano ya primary ya Lurama kwenye Kata ya Bukondo, ukifika tu unajua ukweli hii shule ni chakavu, shule ya Lubanda kwenye Kata ya Busanda ukifika tu unajua shule hii ni chakavu, shule ya Lukumbo katika Kata ya Butundwe ukifika tu unajua shule ni chakavu, hii ni mifano michache tu lakini ziko nyingi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ni ombi langu kwamba, pesa hizi tunazozitoa ziwe ni za kutosha ili kasi ya kurekebisha shule zetu za msingi ionekane kwenye maeneo yetu. Kwa mfano, kuna miradi ya BOOST ambayo ilibajetiwa nafikiri mwaka jana, ukiuliza kule Halmashauri wanakuambia pesa haijafika hadi leo! Sasa kama haijafika maana yake tutakuwa tumewaambia wananchi mwezi wa Nane kwamba kuna BOOST inakuja kurekebisha shule za msingi na pesa haijafika, kwa hiyo kinachoonekana ni Mbunge amesema uwongo nafikiri ndiyo ukweli wenyewe huo, ama Mbunge kasema uongo kwenye eneo lake. Kwa hiyo, niombe sana hizo pesa za BOOST zilizosemwa ziende kufanya kazi ile ili tuwezwe kuhakikisha kwamba yale tuliyoyasema ni sahihi.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni TARURA. Kwenye TARURA hapa kuna kazi kubwa wamefanya inaonekana kazi yao, lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuongeza fedha kwenye Mfuko huu wa TARURA tumeendelea kujenga barabara zetu. Changamoto ambayo nataka kuisema hapa, Mfuko wa TARURA hauna fedha ya dharura, kwa hiyo inapotokea kwa mfano sasa hivi mvua zinanyesha kwenye maeneo mengi, barabara ikiharibika huyu Meneja au Injinia wa TARURA wa Wilaya hana uwezo wa kwenda kufanya kitu chochote atakuambia tusubiri bajeti inayokuja.

Mheshimiwa Spika, sasa kama barabara imekatika watoto hawawezi kwenda shule, bajeti inayokuja itakuja lini? Nina mfano mdogo kwenye eneo langu, barabara kutoka Nyakagwe kwenda Butobela ambako ndiko kuna secondary school daraja limekatika, lakini maelezo yake ni kwamba tutaomba kwenye bajeti inayokuja kwa sababu hana uwezo wa kufanya kitu chochote, watoto wasiende shule?

Mheshimiwa Spika, hivyo, tuone tu namna gani tunaweza kuwa na pesa ya dharura kwenye maeneo hayo ili watoto wetu waendelee kupata huduma kwa utaratibu ule ambao unakubalika. Kama inaonekana fedha ni kidogo siyo vibaya kuiga kama TANROADS walivyo wameingiza EPC+F nao waongeze EPC+F na pesa yao iwe ndogo ili tuweze kufanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alipopita pale kwangu Katoro tuliomba Bilioni 15 kufungua barabara za Katoro, akasema atatoa pesa kidogo kidogo, bahati mbaya sijaziona ninaamini Mheshimiwa Waziri utakuwa umeziandika mahali fulani nisipoziona maana yake nitajua kwamba Mheshimiwa sasa wananchi watakuwa wanasema Mheshimiwa Rais alichokisema siyo sahihi, ningeomba sana ziingie mahali fulani kwa ajili ya kuhakikisha kwamba haya yanawezekana.

Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa ni sekta ya afya. Mwaka juzi tulitembezewa karatasi hapa Bungeni kila mmoja aka-suggest vituo vyake vya afya anavyotaka vijengwe. Mimi niandika vitatu hakijatokea hata kimoja sasa nikawa najiuliza huu ni muujiza au ni kitu gani, kwa sababu niliandika vitatu na hakikutokea hata kimoja. Bahati nzuri sana Kata niliyoiandika kwa mfano Kata ya Lwamgasa ni kwa wachimba madini, kuna wananchi takribani 40,000 kwenye Kata ile, wanahitaji kituo cha afya lakini kituo hakikupatikana. Nikaandika Kata ya pili ya Nyakagomba ina wananchi takribani 30,000 kituo hakikupatikana, nikaandika Kata ya Tatu ya Magenge kuna wananchi karibu takribani 17,000 haikupatikana. Ni kweli inawezekana criteria iliyotumika ilitutoa nje kwamba inahitaji Tarafa, lakini hawa wananchi wote tutawahudumiaje?

Mheshimiwa Spika, ni ombi langu sasa Mheshimiwa Waziri uangalie uwezekano wa vituo hivi tuvipate kwa ajili ya kuhudumia wananchi wetu, wananchi 40,000 hawana kituo cha afya tutawahudumiaje wanahamia kwenda kununua dawa kwenye pharmacy, wanapougua tu wanahisi hii yawezekana ni malaria acha nifanye nini, ninunue dawa tu nipone wengine watakuwa wanapoteza maisha kwa mtindo huo. Kwa hiyo, ni ombi langu Mheshimiwa Waziri kwamba hili utalikumbuka na utaweza kulifanya kazi.

Mheshimiwa Spika, kwenye afya nako tuna maboma, nimeona maboma 300 kwenye ukurasa Namba 21 yanaonekana yamejengwa, kule Busanda yapo maboma mengi tu ya zahanati yamejengwa yanahitaji kumaliziwa, niombe sana kwenye bajeti hii Wizara iangalie uwezekano wa kuyamalizia hayo maboma, yako yaliyoezekwa yanahitaji umaliziaji, yako ambayo hayajaezekwa yanahitaji kumaliziwa tu ili wananchi waendelee kupata huduma.

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa haya niliyoyasema machache kama yakiguswa nitajua hii bajeti kule kwangu watasema ni bajeti ya wananchi. Baada ya maneno haya naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Madini; lakini namshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hii tena ya kuweza kutupa nafasi ya kuchangia Bungeni leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kufanya kazi kubwa ya kuilea Wizara hii, na sasa tunaona maendeleo na ukuaji wa sekta unaendelea kuwa mkubwa. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa yeye, Naibu Waziri na wataalam kwa kusimamia sekta hii kiasi kwamba inaonekana ukuaji wake ni mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaonekana kwenye kumbukumbu kwamba mwaka 2020 ukuaji wake ulikuwa ni asilimia 6.7 lakini sasa mwaka 2021 inaonekana imekuwa inakwenda kwenye asilimia 9.6, maana yake kuna ukuaji, kuna positive gain hapo, kuna positive growth; kwa hiyo tunaamini kwamba kuna kazi kubwa wanayoifanya viongozi wetu hawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye mchango wa Pato la Taifa, napo nilikuwa najaribu kuangalia, inaonekana wamelinganisha vipindi ile first quarter ya mwaka ambayo ndiyo naona imekuja kwenye vitabu vyetu. Kwamba ukienda kwenye mwaka 2020 utaiona 6.7, 2021 utaiona 7.2 na mwaka 2022, kwa kipindi hiki utaiona ni 9.7. Sasa, hapa nilikuwa nataka kushauri, kwamba ikiwezekana wakati mwingine wanapokuja na taarifa hizi, kwa sababu leo tuko kwenye quarter ya tatu tunakaribia ya nne sasa basi tupate data za quarter ya pili ili data za quarter ya kwanza ambazo zinakuwa mpaka 9.7 zinaweza zikawa zimepitwa kidogo na wakati. Tungepata za quarter ya pili zingetuonesha uhalisia wa nini kunaendelea hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati napitia ripoti hii nikilinganisha ninaona kwenye bajeti ambayo walipata mwaka jana takribani bilioni 83.4 na mwaka huu wamepata 89.3. Sasa nikiangalia kwenye maendeleo, mwaka jana tulikuwa na asilimia 26.4, mwaka huu tuna asilimia 25.9 maana yake maendeleo pesa yake inazidi kupungua kwa maana ya pesa nzima inayotolewa lakini bado sekta hii inatakiwa ikue. Kwa hiyo nilitegemea kwa sababu sekta hii inatakiwa ikue basi pesa ya maendeleo mwaka jana ya iwe kidogo ya mwaka huu iwe nyingi. Mwaka huu inaonekana kama ni nyingi kidogo lakini percent yao kwa maana ya pesa ya jumla ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe tu hapo, kwa sababu ndipo mahali ambapo sisi tunaotoka kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo; nishukuru nimepata taarifa leo kwamba asilimia 80 ya madini yanayochangia kwenye Pato hili la Taifa ni dhahabu na mimi natoka sehemu wanayochimba dhahabu. Kwa hiyo nilitegemea kabisa hii pesa ya maendeleo inapoongezeka ndipo fedha ya STAMICO ilipo, ndipo fedha ya GST ilipo wanaoweza kufanya utafiti na kutupatia kanzi data ya madini yako wapi na watu wetu wakachimbe kwa urahisi. Huku ndiko fedha ya STAMICO Ilipo, mahali ambapo wanaweza kununua vifaa vya kwenda kuwasaidia wachimbaji wadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lakini niseme tu kama changamoto, hata mwaka jana niliona STAMICO wamepata mitambo ambayo inasaidia wachimbaji wadogo lakini nikifanya sensa jimboni kwangu wanakochimba sana ni wapi sasa ambako STAMICO wameanza ku-support kwa mitambo ile wachimbaji wadogo, sipaoni. Kwa hiyo niwaombe sana Wizara, inawezekana tukawa na mitambo lakini kwenye utekelezaji, kwenye implementation plan kukawa kuna tatizo. Tumeona kuna mitambo ya bilioni nne lakini bado kwa wananchi hatujaona ile impact kubwa. Kwa hiyo niwaombe sana watu wa STAMICO waende na data za kutuonesha ni wapi wamewasaidia wachimbaji wadogo ili tuweze kupata mchango mkubwa wa pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kitu cha pili ambacho nilitaka nikiseme hapa ni kile ambacho ndugu yangu Kigua alikisema hapa, kuhusu leseni. Mwaka huu tumeshatoa leseni 6,381 na malengo yalikuwa elfu sita mia moja kama sitini na kitu hivi, maana yake tumezidisha lile lengo, maana yake kazi inayofanyika ya kukata leseni ni nzuri sana. Changamoto niliyonayo kama aliyosema mwenzangu asubuhi, hapa kwenye Sheria ya Mineral Right na Sheria ya Surface Right kuna changamoto kubwa. Tunaonekana kabisa mchango kwa Pato la Taifa ni mkubwa na fedha ya madini ni nyingi lakini kiuhalisia wananchi wakaida wanaotoka vijijini wanazidi kuwa maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanazidi kuwa maskini kwa sababu gani? hawa wenye leseni wengi wanaotajwa hapa ni wale wanaoenda kuingia kwenye mfumo huu wa sasa wa kidigitali. Mwananchi wa kawaida kwa elimu ya kawaida huo mfumo hawaujui, na ndugu zangu wanaoshughulikia mtandao hata 3G kule kijijini haipo anawezaje ku access portal ile ilhali 3G haipo? Kwa hiyo kimsingi wanaoweza ku-access ni watu wa mjini. Kwa hiyo leseni zote hizi zitakuwa ni za watu, wajanja wa mjini, na wale wananchi wetu kule chini wakiwa hawana leseni yoyote inayoweza kuwasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana kwenye eneo hili, watu wetu wa ardhi na watu wetu wa madini fanyeni hii surface right na mineral right isomane, ikisomana maana yake tutapunguza haya malalamiko. Mimi mara nyingi huwa nina mifano ya wazi; nimebahatika kutembelea maeneo yanaitwa Kaseme, kata ya Kaseme pale kwetu. Moja ya hoja ambayo waliyokuwa wanazungumzia ni hii. Mtu jioni ameona vimacho macho vya dhahabu eneo lile, asubuhi akiamka anaambiwa kuna mtu alishaingia kwenye mfumo amekatiwa leseni tayari kwa hiyo eneo lile ni la kwake chini kule. Sasa yeye anabaki kuanza kubabaika anaambiwa analipwa shilingi ngapi hajui kwa sababu sheria hizi hazijulikani na elimu hatujatoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niwaombe sana ndugu zangu wa madini, hebu tujikite kutoa elimu kwanza kwa wananchi na tuwafundishe hii portal tunaingiaje. Kwa sababu leo hii nikimpigia mtu yeyote kijijini nikamwambia unaifahamu hiyo portal ya madini wanayoingia anasema hiki ni kitu fulani cha ajabu tu, hakijui. Hebu tuwape elimu hao watu ili kusudi na wao waweze kufaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo wamekaa miaka 20, kesho wanaambiwa mineral right kuna mtu anachimba anamwambia nitakulipa shilingi laki moja moja kila hekari yako moja, ana hekari 29 maana yake analipwa milioni mbili, huyo anayechimba anapata ela ya kutosha lakini huyu mtu anabaki kuwa maskini. Kwa hiyo niwaombe sana ndugu zangu wa madini tutoe elimu kwa wananchi wale wa kawaida ili kusudi wajue nini wafanye kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wanaweza kupata maendeleo kwenye mdini hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikupongeze Mheshimiwa Waziri kwa malengo ambayo umeweka hapa, vipaumbele vyako. Umesema wazi kabisa kwamba unaenda kuwaendeleza wachimbaji wadogo. Nikushukuru vile vile nimeona unakwenda kujenga Jengo la Afisa Madini wa Mkoa wa geita kwa fedha nyingine inayobaki Wizarani. Nikuombe sana, wakati unalijenga hili vile vile tuhakikishe kwamba tunajenga uwezo wa wananchi wetu kuendelea kuchangia kwenye eneo hili. Tukifanya vizuri kwenye eneo hili la madini nina uhakika kuwa mchango wa Taifa badala ya kuwa asilimia kumi utakuwa asilimia 15.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii uliyonipatia ya kuongea katika bajeti hii ya Wizara ya Kilimo. Pia nampongeza sana Mwenyezi Mungu na kumshukuru kwa kutupa nafasi hii ya kuzungumza tena leo katika Bunge hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Waziri wa Kilimo, Naibu Waziri, wataalam, Katibu Mkuu kwa kutupatia bajeti hii ambayo tunaizungumzia leo. Nilivyokuwa napitia nimegundua kwamba ukuaji wa sekta hii sasa uko 3.9. Hapo nyuma ulikuwa 4.9, maana yake kuna mahali fulani ukuaji kama unashuka hivi. Sasa unashuka kwa sababu gani? Nafikiri Waziri atakuja kutuambia, lakini mchango kwa pato la Taifa umekuwa 26.9 na tulikuwa tumekwenda 29, inawezekana kuna sekta imekua inaanza kuchangia zaidi kuliko kilimo. Ikumbukwe tu kwamba sisi Watanzania wengi tumeajiriwa kwenye sekta hii. Kwa hiyo, naamini kabisa ni sekta ambayo inabidi iangaliwe kwa umakini iwe na ukuaji mkubwa, ikikua maana yake na uchumi wetu utakuwa unakua zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka nijikite, naona zile taarifa za kimataifa na za Kitaifa zimezungumziwa sana, nataka nijikite kwenye Halmashauri yetu ya Geita ambayo inaitwa Geita DC. Mwaka 2020 kwenda 2021 sisi tulipanga kulima hekta takribani laki 115.4, lakini tuna hekta laki 327, maana yake tunalima kama asilimia 50 tu. Kuna kitu cha kufanya hapo. Tulitarijia vile vile tuweze kuvuna mazao ya wanga takribani tani laki 364.34 na mazao ya mikunde takribani tani 87,902 kwa kulima hekta 46,245. Hili limefanyika mwaka 2021 na tulipata mazao na ukamilishaji wake asilimia kama 99.9. Mwaka uliofuta makadirio yalikuwa ni hayo hayo na wakapata mafanikio hayo kama asilimia 99.9. Maana yake ni kwamba inawezekana makadirio tunayojiwekea sio makubwa sana kwa sababu eneo kubwa bado halijalimwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ni nini hapo? Inawezekana changomoto hii ya ukuaji wa sekta yetu tunayoiona ni kwa sababu kuna sehemu kubwa kule kwenye maeneo bado haijalimwa. Sasa naishauri nini Serikali? Naishauri Serikali kwamba kwenye mazingira haya tuliyonayo ziko changamoto kadhaa ambazo nazijua nikizitaja kwenye Geita DC zitakuwa ni changamoto ambazo zinaweza kuwa hata ndani ya nchi. Kwa mfano, sisi Jimbo la Geita na Jimbo la Busanda tuna takribani jumla ya kata 37, tuna Maafisa Ugani 23. Unaweza ukajua kama Maafisa Ugani ni 23, kuna kata 14 hazina Maafisa Ugani. Sasa hawa wanaendaje, maana yake ni kwamba hawa wanakwenda bila kuelekezwa nini cha kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano, ukichukua tarafa kwa maana ya Tarafa ya Busanda, kuna kata 11, Maafisa Ugani wako saba. Tarafa ya Butundwe Maafisa Ugani wako tisa, Bugando wako watano, Kasamwa wako wawili jumla ni 23. Tuna kazi kubwa ya kufanya hapo kwamba hawa Maafisa Ugani sasa waongezwe kwenye maeneo yetu. Pia vipimo vya udongo ambavyo mwaka jana tulisema udongo utafitiwe, hakuna kipimo hata kimoja kilichokwenda, maana yake wakulima wetu wanalima kibubu hivi, hawajui udongo una hali gani na kitu gani kinaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha tatu ambacho nilikisema ni pembejeo kwa maana ya mbegu na mbolea. Hii mbolea mfumo uliowekwa mwaka jana na ruzuku iliyowekwa na Rais, nimpongeze Mheshimiwa Rais imeleta uchangamfu wa sekta hii, lakini utaratibu uliotumika, wakulima wengi hawakupata mbolea. Kwa nini? Umbali, kwa hiyo ni ombi langu kwamba sasa mbolea hii ipelekwe kwenye kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ambayo naiona ni kwamba hata wale Mawakala ambao walifanya mwaka jana, wanaonekana sasa hawakwenda vizuri na mfumo wa Serikali, wengine wameanza kwenda TAKUKURU kuhojiwa. Kwa hiyo nina mashaka kwamba utaratibu wa mbolea wa mwaka huu huenda Waziri akapata Mawakala wachache kwa sababu ya hofu hiyo. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri waliangalie hiki tunalifanyaje kwenda kwenye kata zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye mbolea hii hii, wale waliokuwa wameandikishwa mwaka jana wako wakulima wengi hawakuandikishwa. Ningeomba sana hawa waandikishwe ili kusudi kila mmoja aweze kufaidika na hii mbolea ya ruzuku na uzalishaji wetu ukue.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, nimeona kuna upembuzi yakinifu wa skimu kadhaa katika Kata ya Nyakagomba, Kata ya Nyachiluluma, Kata ya Bukondo na Kata ya Magenge. Naamini kabisa hili kama atalifanya kwa wakati huenda tukaona matokeo mapema, kwa sababu tuna takribani hekta 7,200 kwenye maeneo haya ambayo zikiwekewa umwagiliaji watalima mara tatu badala ya kulima mara moja. Kwa hiyo, niombe sana huu upembuzi yakinifu usichukue muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wabunge na nchi nzima tuna matarajio kwa bajeti inayotolewa na Mheshimiwa Rais hapa tuone matokeo mapema na hayo matokeo najua kwa sababu ndio tunaanza yanaweza yakachukua muda mrefu kutokea. Kwa hiyo, niwaombe sana tujitahidi kufanya kadri inavyowezekana matokeo yaanze kuonekana. Kila anayesimama atakuwa anaongelea hili kwa sababu ndio tunaanza na matokeo yanazidi kuchelewa kuoneka, ianze kuonekana nini kinafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ambalo nataka kusema ni kuhusu hizi block farming ambazo wenzangu wamezisema. Kule Mkoani Geita sina uhakika block farming iko sehemu gani. Kwa hiyo kila unayemuuliza anakwambia hiki ni kitu gani. Niwaombe sana hii vocabulary ya block farming hii ije kule Geita watu watambue ni kitu gani kinatakiwa kufanyika, kwa sababu sasa hivi inaonekana tu iko mahali. Najua inawezekana ni kwa sababu ya mafungu, lakini namwomba Mheshimiwa Waziri atembelee kule wamfahamu, wajue block farming ni nini kwa sababu sasa hivi definition yake kule kwetu wanaweza kukwambia ni uvuvi, kumbe block farming ni mashamba. Nimkaribishe sana Waziri aje eneo hilo… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Magessa na muda wako umekwisha, lakini unayo hiari ya kuunga mkono hoja kama ulikua hujamalizia.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga hoja mkono. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana kwa nafasi, hii lakini naomba niseme mambo machache sana kwa sababu ya muda. Pamoja na mambo mengine, uhitaji wa sekta za uzalishaji ikiwemo sekta hii ya kilimo kwa ajili ya ukuaji wa uchumi wa nchi yetu, ni muhimu sana. Kwanza ni kwa sababu asilimia 65 ya Watanzania wameajiriwa na kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tunaamini kwamba tukipata ukuaji mzuri kutoka kwenye hii sekta ya uzalishaji tutaajiri watu wengi; pili, uchumi wetu utakua; tatu, uwezo wa wananchi wetu kustahimili madhara ya mtikisiko wa uchumi wa kidunia ambao unakuja na inflation ambazo wananchi wanashindwa kuzistahimili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa. Mwaka 2021 wakati naongea nilisema Malabo Declaration ilituhitaji tuchangie sekta hii kwa asilimia 10. Mwaka huu tumejitahidi; Mheshimiwa Rais amejitahidi, ni msikivu, ameongeza bajeti kutoka shilingi bilioni 294 kwenda bilioni 751. Niseme wazi kwamba, hii ni hatua moja nzuri sana, lakini bado hatua hii tuliyokwenda nayo haitupeleki kwenye asilimia 10 tuliyoisema, bado tuko mbali kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bilioni 751 niseme wazi kwamba hili ni hatua moja nzuri sana lakini bado hatua hii tuliyokwenda nayo haitupeleki kwenye asilimia 10 tuliyoisema bado tupo mbali kidogo. Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana timu yako. Hoja yetu nataka tuhakikishe kwamba hii sekta ya kilimo inapatiwa fedha ya kutosha ili ukuaji wa uchumi wetu badala yakuwa single digit uwe double digit. Sasa hivi tuna single digit, na unaona inaendelea inacheza inashuka ikicheza inapanda. Tusipowawezesha hawa wananchi wetu kutokana na sekta hizi za uzalishaji hatuwezi kutoka mahali tulipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme wazi, pamoja na pongezi hizi tumeona wazi kwamba kuna ongezeko kwenye utafiti, mahali ambapo tumewapigia kelele sana mwaka jana, kutoka bilioni 7.35 tumeenda bilioni 11.63, umwagiliaji kutoka bilioni 11.5 kwenda bilioni 17.7, lakini mbegu kutoka bilioni 3.42 kwenda bilioni 10.38, haya ndiyo yalikuwa matatizo yetu. Sasa tukiongeza pesa ya kutosha maana yake ongezeko katika maeneo haya niliyoyataja kila atayelima atalima kwenye udongo anaoujua una characteristics gani? Kila atakayelima atalima eneo ambao limewezeshwa skimu za umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi, kwenye umwagiliaji hapo bado kuna shida. Tumeona wazi kwamba ukilima mpunga kwenye skimu za umwagiliaji kutoka tani mbili unapata tani nne au tani tano na unaweza kulima mara mbili kwa mwaka. Sasa, je, skimu tunazo ngapi? Tumeona wazi kabisa kwamba hadi sasa katika hekta milioni 29 sisi lengo letu ilikuwa hekta milioni 1.2 lakini bado tumefikia 700 na kitu tu. Kwa hiyo, bado tupo mbali kidogo kwenye sekta hii ya uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme kutoka kwangu jimboni kwangu. Sisi kwetu kwa upande wa huduma za ugani tuna maafisa ugani 27 na tuna kata 37. Maana yake ni kwamba, kuna kata 10 ambazo hazina ushauri wowote wa kitaalamu. Nimuombe Mheshimiwa Waziri atupatie maafisa ugani watakaoweza kutoa huduma za kigani ambazo zitafanya wananchi wetu waweze kupata mapato yaliyo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliomba mwaka jana kwamba tupate skimu za umwagiliaji, na tukaomba kwaajili ya maeneo ya Saraburwa, Magenge, Nyamaruru pamoja na Nyakagomba, lakini mpaka sasa jimbo langu ninalotoka mimi halina skimu hata moja. Kwa hiyo, haya yanayotajwa kama ndiyo faida za umwagiliaji kwangu kule bado ni ndogo kwasababu hakuna skimu hata moja. Nimuombe sana Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho ahakikisha kwamba kuna skimu fulani inayopatikana jimboni Busanda ili watu wangu pamoja na kupata wakajifunze na waweze kupata uzalishaji huu ambao wenzetu maeneo mengine wanautegemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kusisitiza, pamoja na ongezeko hili bado asilimia 10 ya bajeti yetu iende kwenye kilimo ili tuweze kufanikiwa. Hii tulinayo, ukipiga hesabu utagundua ni one out of six. Kama tuna bilioni arobaini na kitu maana yake ni kwamba tulitegemea tupate trilioni nne. Kwamba kama tuna trilioni 41 tunategemea tupate trilioni ndani ya Sekta ya Uzalishaji, lakini ukipiga hesabu unaona hapa kuna bilioni 751 ukipiga ni one out of six, ambayo kimsingi ukifanya hesabu utagundua hii ni asilimia 16 mpaka 20. Naomba twende kwenye namba, namba hazisemi uongo. Tukienda vizuri naamini kwamba wananchi wetu wataweza kufanikiwa katika eneo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Wizara hii ya Ujenzi, lakini namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo ametupa nafasi ya kuweza kujadili Wizara hii ya Ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, binafsi nijielekeze kuipongeza Serikali kwa mpango mkubwa wa reli ya SGR ambao unatoka Dar es Salaam kuelekea Mwanza, nimeona kuna lot kama tano ambazo zinaendelea kufanyiwa kazi. Kila lot iko kwenye hatua fulani hatua za mwisho, ziko kwenye manunuzi, lakini naomba tu niseme wazi kwamba pamoja na lot hizi inatakiwa tunapotengeneza SGR hii tuone namna Wizara zingine zinavyofanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Wizara yetu ya Kilimo imeongezwa fedha, kwa hiyo, tunaamini kabisa kwamba kuna mazao mengi yanakwenda kuzalishwa kwenye umwagiliaji yatahitaji kupata hii miundombinu ya reli ili yaweze kufanya biashara. Kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hili kwa sababu ninaamini kabisa uzalishaji huu utahitaji kuitumia reli hiyo. Lakini nipongeze tena meli ambazo nimeona meli moja inasemwa iko asilimia 60 ya Ziwa Victoria, MV Mwanza ambayo mkataba ulikuwa unaonesha kwamba ingekamilika mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe tu Mheshimiwa Waziri utakaposimama pamoja na nia njema ya kutengeneza meli hii utuoneshe kwa sababu mwaka huu hatuna uhakika kama asilimia 60 itaweza kumalizika kwa mwaka huu wa fedha. Niombe sana uweze kuonesha hilo ili tuweze kujua kwamba watu wetu wataanza kuhudumiwa na meli hii ya MV Mwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais na Mheshimiwa Waziri na timu yake yote kwa ujenzi wa Daraja la Busisi Kigongo daraja hili limeendelea kujengwa, lakini naiona kama kasi yake ni ndogo, sasa ni ombi langu na niombe kuishauri Serikali iweke usimamizi wa kutosha kuhakikisha kwamba daraja hili linakamilika kwa muda wake ili wananchi wa Kanda ya Ziwa waweze kupata nafasi ya kuvuka sehemu ile ya maji kwenda Geita, kwenda Bukoba na maeneo mengine ambayo yanaweza kuwa na nchi za jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze Mheshimiwa Rais japokuwa kwenye hatua za kwanza mradi wetu wa Rais wa barabara ya kutoka Katoro kuelekea Ushirombo tunategemea unaanza sasa kwamba Bilateral Agreement imeshafanyika na sasa tunatarajia tu kwamba ile technical aspect ya wataalam wetu kutoka kwenye Wizara wataendelea kushughulikia kuhakikisha kwamba barabara hii inajengwa kwa wakati na wananchi wanapata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimpongeze sana Mhandisi Nnko ambaye amekuwa pamoja nasi Mkoani Geita barabara nyingi ambazo anasimamia sasa zinapitika. Niombe tu fedha hizi ambazo zinaonekana zinapitishwa kwenye bajeti hii ziendelee kwenda kule kwa ajili ya kuhakiksiha kwamba wananchi wetu barabara hizi za TANROADS zinaendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini liko moja ambalo sio la barabara, niwapongeze sana ATCL kwamba tulikuwa na shida kama Wabunge unaweza ukaitwa kwenye Kikao cha Halmashauri hapa kutoka Bungeni ikawa changamoto lakini wameanzisha route nzuri ya kutoka hapa kwenda Kanda ya Ziwa ya ndege ambayo inatuchukua hapa kutoka Dodoma kwenda Mwanza na baadaye unaweza kwenda kwenye vikao na baadaye ukaweza kurudi niwapongeze sana kwenye hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pamoja na pongezi zote nilizozitoa sisi kwa maana ya Jimbo la Busanda tumekuwa na changamoto ya barabara ambayo kama wenzangu wanavyosema imeingia kwenye Ilani kila mwaka, kila miaka mitano inakuja lakini haitengenezwi; barabara hii tumekuwa tunaiuliza hapa kila siku barabara hii inatoka Geita - Nyankumbu kwa Mheshimiwa Kanyasu inatakiwa ipite Nyarugusu, ipite Bukoli iende Bulyanhulu pale Kakola halafu iende Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii inashughuli nyingi sana za uchumi kwa watu wa Geita watu zaidi ya milioni mbili wanatakiwa kupita kwenye barabara hiyo, lakini barabara hiyo inapita kwenye migodi midogo midogo mingi maana yake tukiijenga barabara hii watu wetu watapata urahisi wa kufanya shughuli za kiuchumi. Lakini itakuwa ni barabara inayoturahisishia sisi kwenda Dar es Salaam na nchi za jirani kwa maana ya Burundi na Rwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahati mbaya sana mwaka jana niliona ilikuwa imetengewa bilioni karibu tatu, mwaka huu sasa bahati mbaya imetengewa bilioni mbili, maana yake yenyewe kila mwaka pesa yake inazidi kupungua. Kwa hiyo, nikiambiwa ni-predict mwakani itatengewa bilioni moja na mwaka kesho kutwa itakuwa imetengewa sifuri. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Waziri badala ya pesa hii kuonekana inapungua iende inaongezeka na kila tunapoweza kufanya tuisaidie barabara hiyo iweze kujengwa kwa lami kwa ajili ya uzalishaji wa watu wa barabara ile. Ni barabara inayokuja Dar es Salaam na watu wa Geita ni barabara inapitisha makinikia, ni barabara inapitisha mazao mengi ya kutoka Geita kwenda maeneo mengine. Niombe sana Mheshimiwa Waziri utusaidie barabara hii iweze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mwisho kabisa ni barabara hii ya kutoka Mwanza kwenda Bukoba kwenda Chato. Ilipokuwa inajengwa inapita kwenye eneo langu la Katoro, maana yake Jimboni Busanda walisahau kuweka taa, nafikiri wakati huo lot zilikuwa hazitembei na taa kwa hiyo, ukifika eneo lile kuna giza. Niombe sana Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti hii, japokuwa sikuona mahali popote, eneo hilo liwekewe taa ili barabara ile kwenye eneo hilo ambalo ninalisema la kuanzia Kibingo kwenda mpaka Buseresere liwekewe taa ili wananchi waweze kuona, waweze kufanya shughuli zao sio ikifika saa 12:00 jioni biashara imekwisha, iendelee kwa muda kwa sababu kuna taa za barabarani zinaonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mengi ya kuzungumza, lakini Mheshimiwa Waziri naomba haya machache kwa leo yatoshe kufanya bajeti hii niiunge hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii uliyonipatia ya kuchangia mapendekezo ya bajeti kuu, lakini namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa nafasi hii ambayo ameruhusu leo tuweze kuzungumza juu ya bajeti kuu. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa bajeti nzuri ambayo tumeiona, tumeisikiliza. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa hiki ambacho kimeandaliwa na kuletwa kwetu kwa ajili ya kutoa maoni yetu. Naamini kwamba tumeletwa duniani kufanya mambo tunayoyafanya yawe endelevu kwa ajili yetu sisi na vizazi vijavyo. Kwa hiyo, naamini kila tunachokizungumza leo lazima kiwe endelevu kwamba tutakitumia sisi na watu wanaokuja wataendelea kukitumia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, yale tuliyoyakuta tuliyonayo leo na tutakayoyafanya baadaye. Kwa hiyo, naamini kabisa kwa bajeti hii ambayo naiona nilikuwa najaribu kuangalia dhima yake, inatuonesha wazi kwamba, dhima ya bajeti hii ni kuongeza kiasi cha kufufua uchumi na kuimarisha sekta za uzalishaji kwa ajili ya kuboresha maisha. Sasa tunazo sekta za uzalishaji kadhaa ambazo mimi nimekuwa naziangalia kuona kama kuna mabadiliko yamefanyika ili tujue kwamba tunakwenda vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona kwenye madini, ukuaji wa sekta ulitoka asilimia 6.7 kwenda 9.6, lakini kwenye mchango wa Taifa inaonekana inatoka 6.7 kwenda kwenye 7.2, inaoonekana kuna kitu kimefanyika. Sasa tunatakiwa tuhakikishe kwamba utekelezaji wa bajeti hii unakwenda kutupeleka mahali ambapo madini yatakwenda kuchangia pato la Taifa kwa kiwango kikubwa kuliko hiki tulichonacho leo na vilevile ukuaji wa sekta uweze kuongezeka. Ukuaji wa sekta utaongezeka vipi? Utaongezeka kwa sababu tutaongeza wigo wa wale wanaoshughulika na shughuli hizi za madini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mahali nimesikia watu wanazungumzia habari ya makaa ya mawe, inaonekana hayajafanyiwa kazi, yafanyiwe kazi, lakini kuna mahali kwenye maeneo ambayo mimi natoka, jana nilikuwa napigiwa simu na mwanamke mmoja ananiambia, nina plant yangu, nataka umeme nitaupataje? Kwa hiyo, kuna mahali fulani ambapo watu wa umeme sasa wanatakiwa wapeleke umeme kwenye plant hizo ili uzalishaji uongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa haya ni mambo mtambuka, basi Wizara zote ambazo zinahusika kwa mfano watu wa umeme wakaweke umeme kwenye hizo plants ambazo ninazisema ili uzalishaji ule uongezeke. Kwa sababu, tunajua kabisa bajeti ya umeme imeongezeka, haya mambo yatakwenda kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile wale wanaoshughulika na kutoa leseni, Special Mining License, tuongeze wigo huu sasa. Tusichukue muda mrefu sana kuwapatia watu leseni kwa ajili ya kuongeza watu wanaochimba madini. Inawezekana pato letu linaonekana sasa hivi limekua, ni kwa sababu kumetokea mahali fulani mazingira yetu ya vita yale na nini bei yetu ya dhahabu ikapanda au bei ya madini fulani ikapanda, tukaonekana tuna mapato makubwa. Itakapokwenda ku-stabilize mapato yatashuka.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili ambacho nilitaka nikizungumzie ni katika hilo hilo ambalo tumesema, shabaha halisi ya bajeti hii ambayo tunaizungumzia leo imeongezeka. Tunatakiwa kutoka kwenye ukuaji wa 4.7 kwenda at least kwenye 5.3. Kuna mambo fulani ambayo yanatakiwa yafanyike na dhima imeyaonesha wazi. Mfano kilimo, tumepongeza kwa sababu kilimo kimeongezewa zaidi ya Shilingi bilioni mia sita kama na sitini hivi, lakini hoja yangu kubwa hapo ni kwamba, je, machinery yetu iliyozoea kupata Shilingi bilioni 100 tumeiandaa kwa ajili ya kubeba zaidi ya Shilingi bilioni 954? Tusije tukafika mahali tukamtengenezea sifa CAG mwaka kesho akija hapa atuoneshe tu kuna mahali kuna shimo hapa lilitokea, hapa shimo lilitokea. Machinery yetu ya kilimo iko tayari kubeba mzigo huu ambao tumeipatia? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho nilitaka kusema ni sekta ya mifugo na uvuvi ambayo nilitaka niizungumzie. Kilimo wamepata pesa, uvuvi wameongezewa na mifugo ukomo wao kwa Shilingi bilioni 100. Changamoto ninayoiona, sasa nimeona wameandika ukurasa wa 34, wanasema wanakwenda kuchukua Ranch ya Kongwa, hectares 38,000. Sielewi sasa, wakati huo huo kwenye page hiyo wanaonesha wazi kwamba kuna shida, bado mchango wa uvuvi na mifugo haujatosha kwenye Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilitegemea hii Shilingi bilioni 100 iliyoongezeka ikaboreshe NARCO Kongwa, lakini bahati mbaya ni kwamba haiendi kuboresha, wanakwenda kunyang’anywa Kongwa. Sasa sielewi tunakwenda kuboresha mifugo au tuna maana gani? Kwa sababu mapori bado tunayo mengi? Kwa nini wasiende sehemu nyingine tukaiacha Kongwa iboreshwe kwa sababu geographically ranch ilipokuwa located Kongwa pale ni mahali pa kimkakati zaidi. Tukiwaondoa maana yake tumeonesha kwamba, tunawapatia sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa inaonekana tunaondoa mifugo michache iliyo mle ndani, tunaweka mashamba ya alizeti, tunaweka kiwanda cha alizeti kikubwa. Mimi sifikirii kwa sababu tumeongezewa Shilingi bilioni 100, maana yake Shiingi bilioni 40 kwenye mifugo, Shilingi bilioni 60 kwenye uvuvi. Basi twende tukaboreshe maeneo yetu, badala ya kuanza kuyaua sasa, tukiyaua maana yake tutakuwa hatuwezi kwenda. (Makofi)

(Hapa kengele ya kwanza ililia)

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na sekta ya kilimo ambayo nilikuwa naizungumza, tuna maeneo mengi. Maeneo ninayotoka yanapitiwa na Ziwa Viktoria, kwa hiyo, nilitegemea sana hizi irrigation schemes, (hii mifumo ya umwagiliaji) tuione mingi kwenye maeneo hayo ili maji ya Ziwa Viktoria yatumike tujenge uchumi wetu. Sina uhakika sana kama alivyosema mchangiaji aliyepita, tusije tukaja mwaka kesho tunapokuja kuzungumza hapa, tukazungumza kitu kingine tofauti na kile ambacho tumekipanga leo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, kwa sababu nimesikia kengele imelia, nizungumzie wigo huu mpana uluoongezeka wa TIN Number. Tunapigiwa simu nyingi sana sasa kwamba tumerudisha kodi ya kichwa. Kwa hiyo, naona tu kwamba kuna nia njema ya Serikali kama wachangiaji walivyosema huko nyuma kwamba, TIN Number hizi ni muhimu kila mmoja apate Tax Identification Number. Kwa namna yoyote tutakavyofanya, kwa sababu tunataka kuhakikisha kwamba kila mmoja ana TIN Number, elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi wetu ili isionekane kitu kipya kimekuja wananchi wanalalamika wanahisi kama kuna tatizo mbele ya safari, na sisi tukanyamaza kwamba tumeingiza kwenye utaratibu wetu na wananchi wakaona kama wanakwenda kufanyiwa habari ya kodi ya kichwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaamini kabisa Mheshimiwa Waziri kwamba, kitengo kile cha elimu ambacho kipo kwa ndugu zangu wa TRA, kinaweza kwenda kule vijijini kikakaa siku mbili kikarudi Dar es Salaam halafu wanawaambia tumetoa elimu mahali fulani. Ukienda kuuliza elimu yenyewe iliyosemwa huko ndani inaonekena haitoshi. Kwa hiyo, tutumie vyombo vya habari, tutumie majukwaa yote ambayo yanawezekana ili wananchi wapate elimu kwamba TIN Number hii ina maana gani kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maneno haya machache kwa kengele iliyolia naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
The Water Resources Management (Amendment) Act, 2022
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi hii, namshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunipatia nafasi ya kuongea kwenye Bunge hili leo tena. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na timu yake kwa kuja na Muswada huu ambao unakwenda kuimarisha usimamizi wa rasilimali za maji. Wote ni mashahidi kwamba maji yanahitajika kwa kila jamii, yanahitajika kwa ajili ya mifugo, kwa ajili ya kilimo na vitu vingine, kama yataondoka kama alivyochangia Mheshimiwa Kiswaga kutatokea vurugu vita katika awamu hii katika karne inayokuja kwa sababu ya upungufu wa maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili linalofanyika leo ni kitu muhimu sana kwa sababu tunakwenda kusimamia kuhakikisha kwamba rasilimali za maji zitaendelea kuwepo sasa na baadaye. Pia ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri katika Muswada huu nilikuwa najaribu kupitia katika Section Namba 23 mahali ambapo wameonesha wazi kwamba inatakiwa kupatikana elimu, imezungumziwa sana na wenzangu hapa, kama kuna mahali mara nyingi tunakosea ni mahali tunapokwenda kubadilisha, tunapokwenda kuwasimamia wananchi wetu bila kuwapatia elimu kwanza. Hawa wananchi wasipopatiwa elimu mwanzo wanashangaa kitu kipya kimekuja na bado elimu hawajapata, katika hili kwasababu kuna hoja ya awareness, kuna hoja ya elimu kwamba wananchi wanatakiwa wapewe kwenye Section No. 23 nikupongeze sana Mheshimiwa Waziri kwasababu tunakwenda kuwaingia kitu ambacho kitawasaidia katika usimamizi wa rasilimali za maji lakini elimu itakuwa imetolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile ninakupongeza kwenye Section Namba 24 ambayo imeingizwa hapo, inaonesha wazi kwamba kiwango cha elimu au elimu anayotakiwa kuwa nayo mtu ambaye ataajiriwa kuwa Kiongozi wa Bonde La Maji imebainishwa hapo, kuna watu wameonesha Hydrology, Hydro-geology kuna Environmental Engineering na Civil Engineering. Maana yake ni nini kama tunataka kwenda kuwapa watu waongoze mabonde haya na kusimamia maji ni lazima vilevile wayajue maji vizuri ili wanapotoa elimu iwe elimu wanayoijua, kwa hiyo nikupongeze sana kwa hili kwasababu kama unataka kutoa elimu na huyu anayekwenda kutoa elimu hana utaalam hana elimu hiyo atatoa kitu ambacho siyo sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine niseme tu wazi nimekifurahia hapa tena ni kiwango cha uzoefu anaotakiwa kuwa nao huyu Meneja wa Bonde, huko tunapotoka na Waheshimiwa wenzangu wengi, viongozi wa mabonde wamekuwa wanaenda wanawaambia watu wahame kwenye maeneo waliyokuwa wanalima toka wanazaliwa, hii inaleta mkanganyiko maalum, kwa sababu ya uzoefu mtu hajajua anamwambia nini mtu ili aweze kuhama kwenye bonde hilo liendelee kuwa ni sehemu ya chanzo cha maji, sasa ninaamini kabisa kama hawa tunaowapeleka watakuwa wanauzoefu at least wa miaka mitano watakuwa wanajua nini wanakwenda kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Section No. 44 (a) ambayo imeongezwa ambayo inaonesha kwamba kulikuwa sasa inaongezwa Section ambayo inahusiana na watu wanaotumia maji bila vibali, using water without permit. Ni sahihi kwamba Watanzania wengi hapa tulipo tunatumia maji vyovyote vile hata huko tulipo, tunapozaliwa, tunapoishi mimi nikiinuka tu Mheshimiwa Waziri natafuta maji mahali fulani naanza kutumia. Lakini sasa inaonekana kabisa kipengele Namba 44 (a) kimewekwa kwa ajili ya utumiaji wa maji bila kibali. Maana yake sasa maji haya yatadhibitiwa kwamba tunapotaka kuyatumia tunakuwa tunajua kabisa tumetoa kibali hiki kwa ajili ya shughuli fulani na shughuli Fulani, hivyo tunaweza tukawa tume-protect utumiaji wa maji usio sahihi. Lakini Kifungu Namba 44 ambacho kimsingi ndiyo kimetengeneza faini kwamba kuna faini ya mtu ambaye hana kibali lakini kuna faini ya mtu ambaye ametumia maji nje ya utaratibu wa kibali alichopewa, hapa ni mahali muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitaki kupingana na wenzangu waliosema kwamba ukishakuwa na miradi mitatu, ulipewa kibali kwamba haya maji utayatumia kwa ajili ya kunywesha ng’ombe baadaye unasema nitayatumia kwa ajili ya kumwagilia shamba, ni lazima tupate kibali ili tujue usahihi wa utumiaji wa maji haya unajulikana, isionekane kwamba mtu anaibuka tu anasema nimeongeza miradi mitano sasa maji ninatumia hivi hapana. Aombe kibali kingine cha matumizi hayo na hii sheria imeonesha bayana kwenye Section No. 44.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie tu mahali ambapo naweza nikashauri ni hapa ambapo mtu anaonekana amepewa faini lakini analirudia kosa katika section hiyo na inaonekana huyu anapewa adhabu ya Shilingi 100,000 kila anaporudia. Hii Shilingi 100,000 kama ni mfanyabiashara mkubwa anaweza kufanya analysis akagundua kwamba akifanya makosa yale makosa anayoyafanya gharama ya maji ni kubwa kuliko Shilingi 100,000 atarudia tena, kwa hiyo hapa iangaliwe upya ni faini ya aina gani kwa kosa linalojirudia isiendelee kuwa hii Shilingi 100,000 inayofikiriwa, iangaliwe nini kinaweza kufanyika hapo ili kosa hilo lisijirudie.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapongeza sana sheria hii imezungumzia habari ya maabara, watu wetu wengi wanaugua utakuwa mtu anaugua vibarango kichwani, ukimuuliza anatatizo gani anasema watoto wangu walikuwa wanaoga tu maji kutoka kwenye kisima chetu hiki ameugua, maana yake hayo maji hayajatibiwa. Tukiwa na maabara zetu zitaonesha wazi kwamba kuna kasoro ndani ya maji haya, nini kinachokosekana nini kilichozidi, nini ambacho kinaweza kuleta athari kwa mwanadamu na tutakuwa na uhakika kwamba matibabu ya watu wetu kutokana tu na protection yataanza kupatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi wakati tunayafanya haya yote kama Mwenyekiti wangu wa Kamati alivyosema, ni lazima tuhakikishe kwamba Sera yetu ya mwaka 2022 ya Maji imerekebishwa, kwa sababu lazima tuhakikishe kwamba sera inasema nini na sasa tunakwenda kufanya nini, vikipingana maana yake tutakwenda kuleta commotion kwenye mazingira tuliyopo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo inathibitisha kwamba tunatakiwa tuwapatie watu maji ya kutosha, kwa hiyo niseme tu Mheshimiwa Waziri kama alivyochangia Profesa Manya hapo tuhakikishe kwamba wananchi wanapata maji ili upatikanaji wa maji utupe nafasi ya kusimamia vyanzo vya maji bora na maji yaweze kupatikana hata kwa vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja kwa machache haya, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na.2) wa Mwaka 2023
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na. 2) wa Mwaka 2023. Nimpongeze Mwanasheria Mkuu kwa kuja na Muswada huu ambao aliyetangulia ameshagusa sehemu nyingi kuonesha kwamba zipo karibu maeneo matano au sita ambayo yalitakiwa kuguswa na yeye mengi ameyapitia. Mengi yanaonekana yanaongozwa na utaratibu, teknolojia na uhalisia wa mambo ya sasa.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwenye eneo la nguvu za atomic. Tunajua kabisa Tume ya Nguvu za Atom inajaribu ku–control, kujaribu kuratibu mionzi katika mazingira yetu ya kazi. Wako watu wengi kwenye kumbukumbu nyingi utagundua wameathiriwa na mionzi na inawezekana kabisa huko nyuma uratibu haukuwa mzuri sana na ndio sababu nampongeza Mwanasheria kwa sababu ya kuja na hili. Vile vile nampongeza Waziri wa Sheria na Katiba, lakini Kamati yenyewe ambayo imeshughulika kuupitia Muswada huu na kufanya marekebisho na kuruhusu sasa uje kwetu.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Bunge na Wabunge wenzangu ni kupitisha Muswada huu ukawe Sheria kwa ajili ya udhibiti wa mambo mbalimbali ambayo yanaonekana huko ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia Muswada huu wa Nguvu za Atomic, Cap 188, Ibara ya 4, utagundua kwamba yako marekebisho yaliyofanyika hapo. Kwanza umeshughulikia marekebisho katika Kifungu cha 4 na kilichofanyika katika hilo ni kufuta Kifungu kidogo cha (1) na kukiandika upya. Maana yake wamebadilisha zile levels sasa kwenye kifungu hicho kwamba, vitu vyenye viasili vya mionzi na matumizi ya mionzi, vyenye ujazo pungufu zaidi ya becquerel moja kwa gramu na vinakwenda mpaka becquerel kumi kwa gramu. Hivi ukiangalia kwenye Muswada huu vinaonesha kabisa kwamba vitatakiwa kuwa vimeratibiwa.

Mheshimiwa Spika, huko mwanzo kama alivyosema mwenzangu viwango vilikuwa juu, sasa tumeshusha viwango hivi kuhakikisha kwamba uratibu wa vifaa vinavyotoa mionzi au vyenye uasili vya mionzi vinaenda kudhibitiwa ambavyo vimefungwa na ambavyo havijafungwa lakini kwa ujazo huu mdogo. Pia ukiangalia utabaini kwamba imeongezwa ibara ndogo ya tano kwa lengo la kupunguza vile vile uchafuzi wa mazingira yetu kwa njia hii ya mionzi. Kuna mionzi inaitwa Alpha na Beta wale waliosoma sayansi watakuwa wanaijua.

Mheshimiwa Spika, mionzi hii kwenye uso nayo imepunguza kwamba isizidi becquerel 0.8 kwenye uso ambao unaweza kuwa contaminated surface. Sasa hivi ni vitu ambavyo mwanzo vilikuwa havikudhibitiwa na kama havikudhibitiwa wapo watu wengi walikuwa wanaathirika na hili. Kwa hiyo Sheria hii inakuja kuhakikisha kwamba tunaweka sasa uratibu mzuri, watu wetu either wale wanaokuja na vifaa hivyo ambavyo vina mionzi hiyo au wale wanaotumia wasiweze kuathirika kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, ukienda mbele kidogo utagundua (b) kwenye ibara hiyo imeongezwa ibara ndogo ya (7) inayoonesha masharti ya ukomo wa vigezo vya msamaha kuhusu mionzi baada ya kuwa imeidhinishwa na Waziri. Ndugu yangu alisema hapa habari ya compounding, kwamba ni lazima tufike mahali sasa badala ya kwenda tu tunapambana kupeleka mashauri yetu kwenye mahakama. Tufike mahali fulani kuna vitu ambavyo vinaweza kufanyika nje na kama kuna msamaha unaweza kutolewa utolewe lakini utolewe kwa ukomo gani. Hivi navyo vimeainishwa kwenye Sheria hii.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla marekebisho katika ibara hii yanalenga kuweka masharti ya kupunguza viwango vya msamaha kuhusu viwango vya mionzi inayotokana na mmuliko katika vitu mbalimbali ambavyo tunavitumia. Aliyetangulia alisema kuna habari ya simu, niipongeze sana Kamati, nilipongeze Bunge na nimpongeze Spika, kwa nafasi uliyotupatia kwenda pale kwenye Tume ya Mionzi, tumeona vitu vingi na tumeona kabisa watu wengi wanavyoathirika, hata microwave tulizonazo ambazo ni chanzo cha mionzi, ukiiacha wazi tu unaweza ukashangaa baada ya muda unafikiri unachemsha nyama kumbe unamchemsha na yule wa pembeni pale, baada ya muda utagundua ameathirika. Kwa hiyo haya mambo ni mambo muhimu na sisi tuliomba kabisa Tume ile ikiwezekana ije Bungeni hapa, ije ifundishe mambo haya ili watu wasiendelee kununua microwave, kununua vitu vingine na kununua simu kumbe wanaendelea kuathirika bila kujua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ibara ya 5 vilevile imefanyiwa marekebisho katika kifungu cha 11 utaona hapo kumeongezwa maneno kadhaa kama dispose, learned, late lakini vile vile transfer, import kwa sababu kuna watu wanaingiza vitu. Kwa hiyo yameingizwa maneno hayo kwenye Muswada huu, lengo la marekebisho haya ni kuwajumuisha wadau wote wa mionzi hii mbalimbali kupata leseni na kusajiliwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kuna watu wengi wameingia kwenye matumizi ya vifaa ambavyo vinatoa mionzi ya asili au ile ambayo inaonekana inatokana tu na umulikaji lakini hawakuwa wanapata leseni, hapa kwa muswada huu sasa wanatakiwa wawe wamesajiliwa wamepata leseni. Hoja kubwa ni kufanya uratibu wa kutosha kwenye mionzi hii ambayo nimeisema. Iko mionzi ambayo ni ionized na mingine siyo ionized, lakini yote ipo katika mazingira mazuri sana kama utaitumia vibaya kwenye kuathiri. Hata Ndugu zangu wachimbaji wa madini tu huko ninakotoka mimi iko mionzi ya asili unapokwenda kule chini kama haijadhibitiwa vizuri unaweza ukashangaa ndani ya shimo lililoko mionzi ile ikakuletea athari kubwa.

Mheshimiwa Spika, pia ukienda katika Muswada huu utagundua Kifungu katika Ibara ya 10, kulikuwa na neno limeandikwa chakula (food stuff). Hii food stuff ndiyo walikuwa wanaenda kupima mionzi wataalam, lakini kwenye Muswada huu wamebadilisha neno food stuff sasa wanakwenda kwenye food chain, maana yake tutaanza kuipima kwanza mbegu inayoenda kupandwa na ikipimwa ile mbegu sasa tunakuja kwenye process mpaka kwenye chakula chenyewe.

Mheshimiwa Spika, unaweza ukapanda mbegu ikiwa na mionzi, ikakua ikaenda na zao litakalokwenda kutoka mwisho likaja na mionzi. Wewe ukapima ukijua kwamba, tunachopata hapa ni food stuff Hapana! Tunakwenda kuanza kwenye mbegu yenyewe, kama ina mionzi izuiwe kulekule mwanzoni isipandwe. Kwa hiyo, muswada huu ni muswada wa muhimu sana kwa sababu unakwenda kuangalia afya zetu kwa ajili ya kizazi hiki na kizazi kinachokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, yako mambo mengi yaliyoandikwa kwenye Muswada huu, nilitaka kugusa tu kwenye atomi hapo tuweze kujua kwamba, ni muhimu sana kuhakikisha kwamba, Muswada huu unapita kwa sababu ni kawa ajili yetu na vizazi vijavyo.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Miswada hii, takribani mitatu iliyosomwa na Waheshimiwa Mawaziri hapa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, lakini Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, lakini vile vile Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutuletea Miswada mizuri ambayo tunatakiwa kuijadili na hatimaye kuipitisha kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwanza kwenye Muswada wa Sheria huu wa TISS, wa Usalama wa Taifa. Inaonesha wazi kwamba Muswada huu ambao tunauzungumzia sasa hivi tunatakiwa tunapokwenda kuuzungumzia tuusome pamoja na sheria mama ukurasa namba 406. Ukisoma hivi vitu viwili bila kukiacha kimoja unaweza kuuelewa Muswada huu vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu kwa nini tunapendekeza Bunge hili liupitishe ili uanze kufanya kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Usalama wa Taifa wanaendelea kufanya kazi yao na kutuweka katika mazingira salama na viongozi wawe salama.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kwa sababu katika Muswada huu viko vifungu kadhaa, ibara kadhaa ambazo zimewekwa na zimefanyiwa marekebisho kiasi kwamba sasa badala ya kufanyika tu bila kuwa na utaratibu vimeingizwa kwenye sheria. Muswada huu umesema wazi kwamba sasa Mheshimiwa Rais ndiye atakuwa kiongozi wa chombo hiki. Mwanzo anaonekana Mheshimiwa Waziri, watu wote walikuwa wanatakiwa waende kutoa taarifa kwa Mheshimiwa Waziri ambaye alikuwa ndiye mhusika wa Usalama wa Taifa. Kwa Muswada huu inaonekana kwamba sasa hivi kiongozi wa chombo hiki atakuwa ni Mheshimiwa Rais mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo katika ibara ya 5 tunaona wazi kabisa Muswada huu kwa nini napendekeza kwamba upitishwe, wanawekwa rasmi viongozi ambao wanatakiwa kuendelea kulindwa na Usalama wa Taifa. Mwanzo ukiangalia kwenye sheria zilikuwepo, viongozi hawa walilindwa lakini haikuwa rasmi kwenye maandishi kama inavyoonekana leo kwenye Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, tunaona viongozi mbalimbali hapa wakiwa wameandikwa kutokana na vyeo vyao na kama alivyokuwa anasema Mwenyekiti wa Kamati kwamba hata Mwanasheria Mkuu wa Serikali hapa aongezwe ili aweze kupata ulinzi kwa utaratibu huu uliowekwa kwenye sheria hii.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye ibara ya 6 utaona kuna kifungu namba 5A kimeingizwa pale ambacho kinawekwa masharti yanayoonesha wazi kwamba Waziri mhusika atabaki na sheria ya mambo ya kibajeti na mambo ya kisera. Kwa hiyo utaratibu wa Muswada huu unavyoonesha, unaonesha kabisa responsibility matrix yake inatuonesha kwamba Usalama wa Taifa sasa bajeti yao na sera zao zinakuja na Waziri hapa Bungeni. Ukienda kwenye ibara namba 19 ya Muswada huu unaonesha namna ambavyo waajiriwa akiwemo Mkurugenzi Mkuu, wakiwemo waajiriwa wengine wanavyotakiwa kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, hapa ni mahali ambapo panaonesha wazi kwamba viongozi hawa wanatakiwa kuwa na kinga wanapoenda kwenye kazi zao. Hapo kwenye kinga nafikiri kila mmoja anaweza kuwa anafikiria itakuwaje kama hawa watu watakuwa wanakinga wakati wanakwenda kufanya hizi kazi. Nafikiri tumeangalia sheria mbalimbali ndani ya nchi hii, ambazo sheria hizi zinaonesha kabisa kwamba kunapokuwa na good faith lazima kinga iwepo kwa sababu hawa watu wanaenda kufanya kazi ambazo zinawezekana zingine zikawa ni hatarishi, lakini zingine zikawa ni mahali fulani ambapo ni lazima wawe wamekingwa kwa sababu wanaweza kufanya kazi wakapata matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Sheria ya Dawa na Vitendanishi, Sura 219, kifungu cha 118 kinaonesha namna ambavyo huyu mhusika wa dawa hospitali anavyoweza kuwa amefanya kwa good faith hata kama likitokea tatizo asiingizwe kwenye matatizo ya conviction kwamba anaweza kufika mahali akashtakiwa mpaka pale itakapothibitika kwamba alifanya kosa yeye bila good faith.

Mheshimiwa Spika, vilevile Sheria Tasnia ya Nyama ukienda kwenye Sura 421, kifungu cha 14, utakuta kitu kama hicho. Pia ukienda kwenye Sheria ya Viwango, Sheria Na.2 ya mwaka 2019, katika kifungu namba 33(1) napo utakuta vitu kama hivyo. Kwa hiyo utagundua kwamba sheria hii inatuonesha kwamba hawa vijana wetu akiwemo mpaka na Mkurugenzi Mkuu wanapokwenda kwenye kazi zao watakuwa confident, kwamba wanakwenda kufanya kazi, lakini sheria imewalinda kwamba hata kama wakipata matatizo kama wamefanya hii kwenye good faith ikithibitishwa na sheria, hawawezi kuingia kwenye tatizo.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kwa haya machache ambayo nimeyaona, yako mengi ambayo tungeweza kuyapitia kuonesha ubora wa hiki ambacho kimefanyika kwenye sheria hii. Niwaombe sana Wabunge wenzangu tupitishe Muswada huu uwe sheria, ili watu wa Usalama wa Taifa wafanye kazi yao na nchi yetu iendelee kuwa salama. Mtakumbuka wazi ni Muswada huu unaoonesha wazi kwamba viongozi pamoja na kulindwa, kuna vituo ambavyo vitakwenda kulindwa, kuna maeneo yetu ambayo ni very sensitive yatakwenda kulindwa. Ni sheria hii inataja mambo haya. Kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge tunapokwenda kufanya maamuzi, tufanye maamuzi Muswada huu uwe sheria ili uingie katika utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, cha pili, nataka kuzungumzia Tume ya Mipango. Tutakumbuka vizuri mwaka jana tulisema sana juu ya Tume ya Mipango kwamba kuna mipango mingine inagongana, kuna mipango mingine inafanyika leo baada ya wiki mbili inavunjwa na tukaomba ingekuja Tume ya Mipango. Ni kweli kwamba mwaka 2018 kulikuwa na uamuzi na ukabadilishwa, hatusemi ilivunjwa, ilibadilishwa na majukumu yake yakaingizwa kwenye Wizara ya Fedha, ikawa Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, wenyeji wengi wa Dar es Salaam watakumbuka, inaweza ikajengwa barabara baada ya miezi sita wanasema inataka kuja mwendokasi. Barabara imejengwa miezi mitano nyuma, halafu inakuja mwendokasi wanabomoa tena katikati pale. Hii ni pesa ya Serikali. Sasa pesa ya Serikali ambayo unajenga leo halafu baada ya miezi sita unabomoa unasema tena kuna mwendokasi hapa, hiyo gharama ya kwanza inakwenda wapi? Kwa hiyo niwapongeze sana kwanza kwa kuja na mpango huu wa Tume ya Mipango, ambapo sasa mipango yetu itakuwa inajulikana, haitagongaana huko mbele ya safari.

Mheshimiwa Spika, niseme wazi kwamba, tumesoma kwamba Tume ya Mipango inakwenda kufanya tathmini ya utekelezaji wa kile kilichofanyika kwenye Mpango unaokamilika mwaka 2025. Tutapata taarifa kutoka kwenye Tume ya Mipango hii, nini kimefanyika kwa miaka hii 10 iliyopita, ili tuweze kujizatiti wanapokwenda kutengeneza mpango mpya wa 2025 kwenda mwaka 2050. Vile vile imeonesha kwamba kutakuwa na mambo mahususi yanayoenda kusimamiwa na Tume hii. Tuliona wakati tunajadili Muswada huu kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kifungu namba 16(1)(c) utaona kabisa Muswada huu ulikuwa umekuja na kwamba hawa watakuwa vilevile wanakwenda kukusanya mapato, lakini Kamati ilisema wazi hawa wajielekeze kwenye kufanya mipango ya Serikali, wasijielekeze kwenda kwenye kukusanya pesa, tutapoteza ile focus yetu ambayo tunataka sasa hivi Mipango ya Serikali ya muda mfupi na muda mrefu iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kama tutajikita na Tume ya Mipango itafanya kwa utaratibu wa sheria hii ninayoiona hapa, Waheshimia Wabunge tuunge mkono Muswada huu wa Tume ya Mipango uweze kupita uwe sheria. Tuwe na Tume ya Mipango inayopanga mipango ya muda mrefu na mipango ya muda mfupi ili yale ambayo tumeyaona yanagongana, yakionekana Wizara ya Maji, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo, wanafanya kazi moja hiyo hiyo, wanajenga bwawa moja hayataonekana tena.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naomba Wabunge wenzangu waunge mkono, Miswada hii ambayo tumekuja nayo ili iweze kupata kibali cha Wabunge hawa na kuweza kuwa sheria. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia kwenye Miswada hii, takribani mitatu iliyosomwa na Waheshimiwa Mawaziri hapa. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, lakini Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria, lakini vile vile Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kutuletea Miswada mizuri ambayo tunatakiwa kuijadili na hatimaye kuipitisha kwa ajili ya maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, nitajikita kwanza kwenye Muswada wa Sheria huu wa TISS, wa Usalama wa Taifa. Inaonesha wazi kwamba Muswada huu ambao tunauzungumzia sasa hivi tunatakiwa tunapokwenda kuuzungumzia tuusome pamoja na sheria mama ukurasa namba 406. Ukisoma hivi vitu viwili bila kukiacha kimoja unaweza kuuelewa Muswada huu vizuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, Muswada huu kwa nini tunapendekeza Bunge hili liupitishe ili uanze kufanya kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Usalama wa Taifa wanaendelea kufanya kazi yao na kutuweka katika mazingira salama na viongozi wawe salama.

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kwa sababu katika Muswada huu viko vifungu kadhaa, ibara kadhaa ambazo zimewekwa na zimefanyiwa marekebisho kiasi kwamba sasa badala ya kufanyika tu bila kuwa na utaratibu vimeingizwa kwenye sheria. Muswada huu umesema wazi kwamba sasa Mheshimiwa Rais ndiye atakuwa kiongozi wa chombo hiki. Mwanzo anaonekana Mheshimiwa Waziri, watu wote walikuwa wanatakiwa waende kutoa taarifa kwa Mheshimiwa Waziri ambaye alikuwa ndiye mhusika wa Usalama wa Taifa. Kwa Muswada huu inaonekana kwamba sasa hivi kiongozi wa chombo hiki atakuwa ni Mheshimiwa Rais mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hilo katika ibara ya 5 tunaona wazi kabisa Muswada huu kwa nini napendekeza kwamba upitishwe, wanawekwa rasmi viongozi ambao wanatakiwa kuendelea kulindwa na Usalama wa Taifa. Mwanzo ukiangalia kwenye sheria zilikuwepo, viongozi hawa walilindwa lakini haikuwa rasmi kwenye maandishi kama inavyoonekana leo kwenye Muswada huu.

Mheshimiwa Spika, tunaona viongozi mbalimbali hapa wakiwa wameandikwa kutokana na vyeo vyao na kama alivyokuwa anasema Mwenyekiti wa Kamati kwamba hata Mwanasheria Mkuu wa Serikali hapa aongezwe ili aweze kupata ulinzi kwa utaratibu huu uliowekwa kwenye sheria hii.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye ibara ya 6 utaona kuna kifungu namba 5A kimeingizwa pale ambacho kinawekwa masharti yanayoonesha wazi kwamba Waziri mhusika atabaki na sheria ya mambo ya kibajeti na mambo ya kisera. Kwa hiyo utaratibu wa Muswada huu unavyoonesha, unaonesha kabisa responsibility matrix yake inatuonesha kwamba Usalama wa Taifa sasa bajeti yao na sera zao zinakuja na Waziri hapa Bungeni. Ukienda kwenye ibara namba 19 ya Muswada huu unaonesha namna ambavyo waajiriwa akiwemo Mkurugenzi Mkuu, wakiwemo waajiriwa wengine wanavyotakiwa kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, hapa ni mahali ambapo panaonesha wazi kwamba viongozi hawa wanatakiwa kuwa na kinga wanapoenda kwenye kazi zao. Hapo kwenye kinga nafikiri kila mmoja anaweza kuwa anafikiria itakuwaje kama hawa watu watakuwa wanakinga wakati wanakwenda kufanya hizi kazi. Nafikiri tumeangalia sheria mbalimbali ndani ya nchi hii, ambazo sheria hizi zinaonesha kabisa kwamba kunapokuwa na good faith lazima kinga iwepo kwa sababu hawa watu wanaenda kufanya kazi ambazo zinawezekana zingine zikawa ni hatarishi, lakini zingine zikawa ni mahali fulani ambapo ni lazima wawe wamekingwa kwa sababu wanaweza kufanya kazi wakapata matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Sheria ya Dawa na Vitendanishi, Sura 219, kifungu cha 118 kinaonesha namna ambavyo huyu mhusika wa dawa hospitali anavyoweza kuwa amefanya kwa good faith hata kama likitokea tatizo asiingizwe kwenye matatizo ya conviction kwamba anaweza kufika mahali akashtakiwa mpaka pale itakapothibitika kwamba alifanya kosa yeye bila good faith.

Mheshimiwa Spika, vilevile Sheria Tasnia ya Nyama ukienda kwenye Sura 421, kifungu cha 14, utakuta kitu kama hicho. Pia ukienda kwenye Sheria ya Viwango, Sheria Na.2 ya mwaka 2019, katika kifungu namba 33(1) napo utakuta vitu kama hivyo. Kwa hiyo utagundua kwamba sheria hii inatuonesha kwamba hawa vijana wetu akiwemo mpaka na Mkurugenzi Mkuu wanapokwenda kwenye kazi zao watakuwa confident, kwamba wanakwenda kufanya kazi, lakini sheria imewalinda kwamba hata kama wakipata matatizo kama wamefanya hii kwenye good faith ikithibitishwa na sheria, hawawezi kuingia kwenye tatizo.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kwa haya machache ambayo nimeyaona, yako mengi ambayo tungeweza kuyapitia kuonesha ubora wa hiki ambacho kimefanyika kwenye sheria hii. Niwaombe sana Wabunge wenzangu tupitishe Muswada huu uwe sheria, ili watu wa Usalama wa Taifa wafanye kazi yao na nchi yetu iendelee kuwa salama. Mtakumbuka wazi ni Muswada huu unaoonesha wazi kwamba viongozi pamoja na kulindwa, kuna vituo ambavyo vitakwenda kulindwa, kuna maeneo yetu ambayo ni very sensitive yatakwenda kulindwa. Ni sheria hii inataja mambo haya. Kwa hiyo niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge tunapokwenda kufanya maamuzi, tufanye maamuzi Muswada huu uwe sheria ili uingie katika utekelezaji.

Mheshimiwa Spika, cha pili, nataka kuzungumzia Tume ya Mipango. Tutakumbuka vizuri mwaka jana tulisema sana juu ya Tume ya Mipango kwamba kuna mipango mingine inagongana, kuna mipango mingine inafanyika leo baada ya wiki mbili inavunjwa na tukaomba ingekuja Tume ya Mipango. Ni kweli kwamba mwaka 2018 kulikuwa na uamuzi na ukabadilishwa, hatusemi ilivunjwa, ilibadilishwa na majukumu yake yakaingizwa kwenye Wizara ya Fedha, ikawa Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Spika, wenyeji wengi wa Dar es Salaam watakumbuka, inaweza ikajengwa barabara baada ya miezi sita wanasema inataka kuja mwendokasi. Barabara imejengwa miezi mitano nyuma, halafu inakuja mwendokasi wanabomoa tena katikati pale. Hii ni pesa ya Serikali. Sasa pesa ya Serikali ambayo unajenga leo halafu baada ya miezi sita unabomoa unasema tena kuna mwendokasi hapa, hiyo gharama ya kwanza inakwenda wapi? Kwa hiyo niwapongeze sana kwanza kwa kuja na mpango huu wa Tume ya Mipango, ambapo sasa mipango yetu itakuwa inajulikana, haitagongaana huko mbele ya safari.

Mheshimiwa Spika, niseme wazi kwamba, tumesoma kwamba Tume ya Mipango inakwenda kufanya tathmini ya utekelezaji wa kile kilichofanyika kwenye Mpango unaokamilika mwaka 2025. Tutapata taarifa kutoka kwenye Tume ya Mipango hii, nini kimefanyika kwa miaka hii 10 iliyopita, ili tuweze kujizatiti wanapokwenda kutengeneza mpango mpya wa 2025 kwenda mwaka 2050. Vile vile imeonesha kwamba kutakuwa na mambo mahususi yanayoenda kusimamiwa na Tume hii. Tuliona wakati tunajadili Muswada huu kwenye Kamati.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kifungu namba 16(1)(c) utaona kabisa Muswada huu ulikuwa umekuja na kwamba hawa watakuwa vilevile wanakwenda kukusanya mapato, lakini Kamati ilisema wazi hawa wajielekeze kwenye kufanya mipango ya Serikali, wasijielekeze kwenda kwenye kukusanya pesa, tutapoteza ile focus yetu ambayo tunataka sasa hivi Mipango ya Serikali ya muda mfupi na muda mrefu iweze kutekelezwa.

Mheshimiwa Spika, naamini kabisa kama tutajikita na Tume ya Mipango itafanya kwa utaratibu wa sheria hii ninayoiona hapa, Waheshimia Wabunge tuunge mkono Muswada huu wa Tume ya Mipango uweze kupita uwe sheria. Tuwe na Tume ya Mipango inayopanga mipango ya muda mrefu na mipango ya muda mfupi ili yale ambayo tumeyaona yanagongana, yakionekana Wizara ya Maji, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Mifugo, wanafanya kazi moja hiyo hiyo, wanajenga bwawa moja hayataonekana tena.

Mheshimiwa Spika, baada ya maneno hayo, naomba Wabunge wenzangu waunge mkono, Miswada hii ambayo tumekuja nayo ili iweze kupata kibali cha Wabunge hawa na kuweza kuwa sheria. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Ubia Baina ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi wa Mwaka 2023
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipatia nafasi hii ya kupitia Muswada wa Sheria wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa mwaka 2023. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa fursa hii ambayo anatupatia ya kujadiliana mambo makubwa ya Sheria zetu na kupitisha sheria mbalimbali na marekebisho mbalimbali ambayo tunayafanya hapa. Nimpongeze Waziri wa Fedha kwa kuja na PPP lakini nimpongeze Mwanasheria Mkuu kwa kutuletea Muswada huu ambao una marekebisho ya Sheria takribani nane hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Sheria ya Usajili na Ubunifu wa Majengo na Wakadiriaji wa Majengo Sura ya 269 lakini tuna Sheria ya Huduma za Habari Sura 229, Sheria ya Bohari ya Dawa Sura 70, Sheria ya Mazishi ya Viongozi wa Kitaifa Sura 419, tuna Sheria ya Reli Sura 170, Sheria ya Utafiti wa Misitu Tanzania Sura 277 lakini tuna Sheria ya Mamlaka na Majukumu ya Msajili wa Hazina Sura 370 na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani Sura 148.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana kwamba Bunge hili, nishauri tu hata kabla sijazungumza kwamba kama Kamati tumepitia, tumechukua muda mrefu kujadiliana juu ya Miswada hii ambayo imekuja na marekebisho makubwa tumeyafanya. Niwapongeze sana Mawaziri, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye amekuja na tumemhoji na tumefikia mahali ambapo tumekuja na kitu ambacho sasa naamini kwamba Wabunge wenzangu niwashawishi tu kwamba tufanye mabadiliko haya ili Sheria hizi ziende kutumika kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita sehemu chache katika mabadiliko au marekebisho haya. Sheria ya Huduma ya Habari Sura 229; Ukipita kwenye Sheria hii utagundua kuna marekebisho makubwa yamefanyika kama walivyosema wenzangu ya kumpunguzia madaraka au mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Maelezo, kumpungizia juu ya jukumu la utartibu wa matangazo yote ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana kama walivyosema wenzangu kwamba alikuwa na madaraka makubwa na hivyo matangazo yote yalitakiwa yatoke kutoka kwenye kiti hicho cha Mkurugenzi Mkuu wa Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili, vilevile imeeleza Serikali kuwa na uhuru wa kuchagua chombo gani kinaweza kutumika kufanya matangazo. Lakini kingine ambacho kimefanyika ni kwamba Muswada umependekeza kufuta kifungu namba 38(3) kilichokuwa kimeweka masharti ya mtu kushtakiwa kwa makosa ya kijinai. Hawa waandishi wa habari walikuwa wanashtakiwa na makosa ya kijinai au ya madai pale tu ambapo anaonekana ameshughulika kutoa taarifa zinazodhaniwa kuwa zisizoweza kuingiliwa (absolutely privileged).

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kifungu hiko kinaenda kufutwa ili kuhakikisha kwamba hawa sasa wanapata haki ya uhuru wa maoni. Kwa hiyo, niseme tu wazi kwamba kuna haki ya uhuru wa maoni inakwenda kufanyika kwenye eneo hili. Waandishi wa habari wajiandae sasa kwa sababu haki hii imepanuliwa na marekebisho ya Muswada huu. Vile vile, mapendekezo ya marekebisho ya kwenye vifungu vya 50 hadi 55 na vifungu namba 63 na 64 ambavyo vinahakikisha wanahabari wanafurahia haki ya uhuru wa maoni yao. Kwa hiyo, niseme tu wazi, kama kuna mahali wanahabari waliona kwamba walikuwa hawana uhuru na haki ya maoni sasa wanakwenda kuipata baada ya marekebisho haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walivyokuja walikuja na maoni takribani 21 lakini nimpongeze Waziri wa Habari kwamba haya yote 21 yamefanyiwa kazi na sasa hata yale ambayo yanaonekana kwenye Sheria hayajarekebishwa yatakwenda kwenye kanuni kufanyiwa marekebisho. Kwa hiyo, nimpongeze sana Waziri kwa hili. Lakini niipongeze vile vile kuja na Sheria hii ambayo sasa inakwenda kufanya watu wetu wawe na uhuru wa kutoa maoni yao na wananchi wapate habari kama ilivyotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho nilitaka kusema hapa ni kile ambacho na wenzangu wamekwishakisema. Mtu ana mashine zake za kudurufu kutoa matangazo. Wakati anapewa adhabu na zile mashine nazo zinakuwa zimepewa adhabu kwa sababu wanasema nazo zimefungiwa ilhali mwenye mashine hizi hawezi kujua maudhui ya kile ambacho kinakuja kuchapishwa hapa. Kwa hiyo, kwenye Sheria hii inaonesha wazi kwamba sasa mashine zile hazitakuwa zimeingizwa kwenye hilo ambalo tunalisema. Kwa mazingira hayo maana yake ni kwamba wananchi hawa na wamiliki wa mali hizi wamepewa nafasi kubwa ya kuchapisha habari yoyote wakati mashine zao hazitaweza kufungiwa.

Mheshimiwa Naibu spika, lakini kingine kimesemwa ni habari ya leseni, kwamba leseni kwa nini inakuwa ya mwaka mmoja. Tumelihoji hili kwa nini mwaka mmoja? Kuna watu wana maduka yana thamani kule Kariakoo ya karibu bilioni moja wanakata leseni kila mwaka, sasa kwa nini hawa watu wasikate leseni kila mwaka? Lakini kitaalamu tu bado hoja ya leseni vile vile inaweza kuwa ni investment, initial investment. Kwamba kama investment ni kubwa tunaamini kabisa huyu leseni yake inaweza kuwa inachukua muda mrefu sana. Kwa hiyo, ninaamini ziko investments nyingine ambazo unaweza ukaziona tulisema tu na maduka mahali fulani yanafanyika ya milioni 500 mulioni 600. Wapate hiyo license tuwa-comply, kila mwaka. Kwa hiyo, niseme wazi tu tusifikirie tu kwamba unaweza ukampatia. Magazeti ambayo mimi nazaliwa niliyakuta leo hayapo. Wangepewa leseni ya miaka 200 ingekuwaje? ingetuletea shida Kwa hiyo, naomba tu waendele kukata leseni kila mwaka ili waendelee kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumzia hii habari ya hii Sheria yetu ya habari ninaomba nijikite kidogo kwenye eneo la reli. Ukiangalia kwenye eneo la reli kwenye Sheria yetu ya leo Sura namba 170 hapa wafanyabiashara binafsi wanaingia kuanza kuchangia, kulipa kama ni ada na kulipa mchango wote ambao utatakiwa kufanyika kwenye reli tulizonazo. Ukiangalia sisi huko nyuma hatukuwa na hii kitu, reli iliyokuwa inapita ni reli ya wananchi na treni inayopita ni treni ya wananchi. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba kile ambacho tulitegemea kwamba tunaweza kuwa na treni mbili kutoka Kigoma zikaja Dar es Salaam utakuta inatoka treni moja kila siku, lakini kumbe tuna uwezo wa kutoa treni tatu kama PPP ambayo tumeisema leo hawa watajiunga na kuingia kufanya shughuli hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Sheria ya Reli kwenye ibara namba 38 na 52 imefanya mrekebisho haya; na ibara namba 46 inawezesha sasa kama kuna mtu mwenye nia ya kutumia maeneo ya reli kuomba kibali kwa shirika na kulipa ada pamoja na gharama zinazohusiana na matumizi hayo. Kwa hiyo, tunaamini kabisa hata Waheshimiwa Wabunge ambao wanataka sasa kununua treni zao ni muda wao sasa lakini kama Mbunge unaona huwezi kununua treni au mwananchi hawezi kununua treni, nunua mabehewa ni muda wako sasa tunataka watu wafanye biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine kwenye ibara namba 52 tunaongeza kifungu namba 108 (5) kinaonesha wazi kwamba kuna masharti mtu yoyote ambaye anataka kuweka kuna mahali kunaitwa railway crossing barabra ina-cross na treni; barabara na Reli na unataka kuweka hiyo, wanasema tayari kwenye mabadiliko haya ya Sheria, kazi yako wewe ni Kwenda kuomba kibali. Kibali kile kitakupa nafasi ya wewe kama unazo fedha kufanya hicho kitu kwa kulinganisha na kile ambacho unatakiwa kulipa kwa gharama ulizo nazo wewe Kwa hiyo, ninaamini kabisa kwa mazingira haya, sasa wawekezaji wetu wana nafasi kubwa ya kuchangia kwenye uchumi wetu kwa sababu reli hii tunayojenga kama ni SGR au reli hii ambayo tunatumia ya zamani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Magessa kengele ya pili, ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja.
The Written Laws (Miscellaneous Amendments) Act, 2023
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipatia nafasi hii ya kupitia Muswada wa Sheria wa Marekebisho ya Sheria Mbalimbali wa mwaka 2023. Nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa fursa hii ambayo anatupatia ya kujadiliana mambo makubwa ya Sheria zetu na kupitisha sheria mbalimbali na marekebisho mbalimbali ambayo tunayafanya hapa. Nimpongeze Waziri wa Fedha kwa kuja na PPP lakini nimpongeze Mwanasheria Mkuu kwa kutuletea Muswada huu ambao una marekebisho ya Sheria takribani nane hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Sheria ya Usajili na Ubunifu wa Majengo na Wakadiriaji wa Majengo Sura ya 269 lakini tuna Sheria ya Huduma za Habari Sura 229, Sheria ya Bohari ya Dawa Sura 70, Sheria ya Mazishi ya Viongozi wa Kitaifa Sura 419, tuna Sheria ya Reli Sura 170, Sheria ya Utafiti wa Misitu Tanzania Sura 277 lakini tuna Sheria ya Mamlaka na Majukumu ya Msajili wa Hazina Sura 370 na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani Sura 148.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze sana kwamba Bunge hili, nishauri tu hata kabla sijazungumza kwamba kama Kamati tumepitia, tumechukua muda mrefu kujadiliana juu ya Miswada hii ambayo imekuja na marekebisho makubwa tumeyafanya. Niwapongeze sana Mawaziri, Mwanasheria Mkuu wa Serikali ambaye amekuja na tumemhoji na tumefikia mahali ambapo tumekuja na kitu ambacho sasa naamini kwamba Wabunge wenzangu niwashawishi tu kwamba tufanye mabadiliko haya ili Sheria hizi ziende kutumika kwa ajili ya maendeleo ya watu wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajikita sehemu chache katika mabadiliko au marekebisho haya. Sheria ya Huduma ya Habari Sura 229; Ukipita kwenye Sheria hii utagundua kuna marekebisho makubwa yamefanyika kama walivyosema wenzangu ya kumpunguzia madaraka au mamlaka Mkurugenzi wa Idara ya Maelezo, kumpungizia juu ya jukumu la utartibu wa matangazo yote ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, inawezekana kama walivyosema wenzangu kwamba alikuwa na madaraka makubwa na hivyo matangazo yote yalitakiwa yatoke kutoka kwenye kiti hicho cha Mkurugenzi Mkuu wa Habari.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha pili, vilevile imeeleza Serikali kuwa na uhuru wa kuchagua chombo gani kinaweza kutumika kufanya matangazo. Lakini kingine ambacho kimefanyika ni kwamba Muswada umependekeza kufuta kifungu namba 38(3) kilichokuwa kimeweka masharti ya mtu kushtakiwa kwa makosa ya kijinai. Hawa waandishi wa habari walikuwa wanashtakiwa na makosa ya kijinai au ya madai pale tu ambapo anaonekana ameshughulika kutoa taarifa zinazodhaniwa kuwa zisizoweza kuingiliwa (absolutely privileged).

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kifungu hiko kinaenda kufutwa ili kuhakikisha kwamba hawa sasa wanapata haki ya uhuru wa maoni. Kwa hiyo, niseme tu wazi kwamba kuna haki ya uhuru wa maoni inakwenda kufanyika kwenye eneo hili. Waandishi wa habari wajiandae sasa kwa sababu haki hii imepanuliwa na marekebisho ya Muswada huu. Vile vile, mapendekezo ya marekebisho ya kwenye vifungu vya 50 hadi 55 na vifungu namba 63 na 64 ambavyo vinahakikisha wanahabari wanafurahia haki ya uhuru wa maoni yao. Kwa hiyo, niseme tu wazi, kama kuna mahali wanahabari waliona kwamba walikuwa hawana uhuru na haki ya maoni sasa wanakwenda kuipata baada ya marekebisho haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, walivyokuja walikuja na maoni takribani 21 lakini nimpongeze Waziri wa Habari kwamba haya yote 21 yamefanyiwa kazi na sasa hata yale ambayo yanaonekana kwenye Sheria hayajarekebishwa yatakwenda kwenye kanuni kufanyiwa marekebisho. Kwa hiyo, nimpongeze sana Waziri kwa hili. Lakini niipongeze vile vile kuja na Sheria hii ambayo sasa inakwenda kufanya watu wetu wawe na uhuru wa kutoa maoni yao na wananchi wapate habari kama ilivyotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho nilitaka kusema hapa ni kile ambacho na wenzangu wamekwishakisema. Mtu ana mashine zake za kudurufu kutoa matangazo. Wakati anapewa adhabu na zile mashine nazo zinakuwa zimepewa adhabu kwa sababu wanasema nazo zimefungiwa ilhali mwenye mashine hizi hawezi kujua maudhui ya kile ambacho kinakuja kuchapishwa hapa. Kwa hiyo, kwenye Sheria hii inaonesha wazi kwamba sasa mashine zile hazitakuwa zimeingizwa kwenye hilo ambalo tunalisema. Kwa mazingira hayo maana yake ni kwamba wananchi hawa na wamiliki wa mali hizi wamepewa nafasi kubwa ya kuchapisha habari yoyote wakati mashine zao hazitaweza kufungiwa.

Mheshimiwa Naibu spika, lakini kingine kimesemwa ni habari ya leseni, kwamba leseni kwa nini inakuwa ya mwaka mmoja. Tumelihoji hili kwa nini mwaka mmoja? Kuna watu wana maduka yana thamani kule Kariakoo ya karibu bilioni moja wanakata leseni kila mwaka, sasa kwa nini hawa watu wasikate leseni kila mwaka? Lakini kitaalamu tu bado hoja ya leseni vile vile inaweza kuwa ni investment, initial investment. Kwamba kama investment ni kubwa tunaamini kabisa huyu leseni yake inaweza kuwa inachukua muda mrefu sana. Kwa hiyo, ninaamini ziko investments nyingine ambazo unaweza ukaziona tulisema tu na maduka mahali fulani yanafanyika ya milioni 500 mulioni 600. Wapate hiyo license tuwa-comply, kila mwaka. Kwa hiyo, niseme wazi tu tusifikirie tu kwamba unaweza ukampatia. Magazeti ambayo mimi nazaliwa niliyakuta leo hayapo. Wangepewa leseni ya miaka 200 ingekuwaje? ingetuletea shida Kwa hiyo, naomba tu waendele kukata leseni kila mwaka ili waendelee kufanya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuzungumzia hii habari ya hii Sheria yetu ya habari ninaomba nijikite kidogo kwenye eneo la reli. Ukiangalia kwenye eneo la reli kwenye Sheria yetu ya leo Sura namba 170 hapa wafanyabiashara binafsi wanaingia kuanza kuchangia, kulipa kama ni ada na kulipa mchango wote ambao utatakiwa kufanyika kwenye reli tulizonazo. Ukiangalia sisi huko nyuma hatukuwa na hii kitu, reli iliyokuwa inapita ni reli ya wananchi na treni inayopita ni treni ya wananchi. Kwa hiyo, matokeo yake ni kwamba kile ambacho tulitegemea kwamba tunaweza kuwa na treni mbili kutoka Kigoma zikaja Dar es Salaam utakuta inatoka treni moja kila siku, lakini kumbe tuna uwezo wa kutoa treni tatu kama PPP ambayo tumeisema leo hawa watajiunga na kuingia kufanya shughuli hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Sheria ya Reli kwenye ibara namba 38 na 52 imefanya mrekebisho haya; na ibara namba 46 inawezesha sasa kama kuna mtu mwenye nia ya kutumia maeneo ya reli kuomba kibali kwa shirika na kulipa ada pamoja na gharama zinazohusiana na matumizi hayo. Kwa hiyo, tunaamini kabisa hata Waheshimiwa Wabunge ambao wanataka sasa kununua treni zao ni muda wao sasa lakini kama Mbunge unaona huwezi kununua treni au mwananchi hawezi kununua treni, nunua mabehewa ni muda wako sasa tunataka watu wafanye biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine kwenye ibara namba 52 tunaongeza kifungu namba 108 (5) kinaonesha wazi kwamba kuna masharti mtu yoyote ambaye anataka kuweka kuna mahali kunaitwa railway crossing barabra ina-cross na treni; barabara na Reli na unataka kuweka hiyo, wanasema tayari kwenye mabadiliko haya ya Sheria, kazi yako wewe ni Kwenda kuomba kibali. Kibali kile kitakupa nafasi ya wewe kama unazo fedha kufanya hicho kitu kwa kulinganisha na kile ambacho unatakiwa kulipa kwa gharama ulizo nazo wewe Kwa hiyo, ninaamini kabisa kwa mazingira haya, sasa wawekezaji wetu wana nafasi kubwa ya kuchangia kwenye uchumi wetu kwa sababu reli hii tunayojenga kama ni SGR au reli hii ambayo tunatumia ya zamani…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Magessa kengele ya pili, ahsante kwa mchango mzuri.

MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naomba kuunga mkono hoja.