Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon. Simon Songe Lusengekile (11 total)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE Aliuliza:-

Je, ni lini Mradi wa Maji wa Nyashimo, Kata ya Nyashimo ambao ulitegemewa kukamilika mwezi Oktoba, 2020 utakamilika ili wananchi waweze kupata maji safi na salama?
NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwa niaba ya Waziri wa Maji naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Maji Nyashimo ulianza kutekelezwa mwezi Julai, 2019 na ulitegemewa kukamilika tarehe Oktoba, 2020 kwa gharama ya shilingi bilioni 1.58. Wakati utekelezaji wa mradi, Mkandarasi alipata changamoto zilizosababisha kuomba kuongezewa muda na hivyo mradi huu unatekelezwa kufikia mwaka huu 4 Aprili, 2021 ambapo ombi lake lillikubaliwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa utekelezaji wa mradi huo upo katika hatua ya majaribio ya kusukuma maji kupeleka kwenye tanki baada ya kufanikiwa kufunga umeme tarehe 9 Januari, 2021. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Aprili, 2021 na kuhudumia wakazi wapatao 12,000. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU K.n.y. MHE. SIMON S. LUSENGEKILE Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka vifaa katika Hospitali ya Wilaya ya Busega ili huduma bora za afya ziendelee kutolewa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Busega ni miongoni mwa hospitali 67 za Halmashauri zilizoanza kujengwa mwaka 2018/2019 kwa kupewa fedha kiasi cha shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa majengo saba ambayo ni jengo la utawala, jengo la wagonjwa wa nje, jengo la maabara, jengo la mionzi, jengo la wazazi, jengo la kufulia na jengo la kuhifadhia dawa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi wa hospitali 67 za Halmashauri ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Busega ambayo imetengewa shilingi milioni 500.

Vilevile katika mwaka wa fedha 2020/2021 Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 33.5 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba katika hospitali 67 za Halmashauri ikiwemo Hospitali ya Halmashauri ya Busega ambayo imetengewa shilingi milioni 500.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza:-

Wananchi wa Kata ya Imalamate Wilayani Busega wamejenga zahanati na kumaliza maboma manne kwa maana ya zahanati moja kila kijiji:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia wananchi hao kuezeka maboma hayo ili waweze kupata huduma za afya kwenye zahanati hizo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya huduma za afya katika Wilaya ya Busega, ambapo katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukarabati wa Kituo cha Afya Nasa na kukiwezesha kuanza kutoa huduma za dharura za upasuaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 Serikali iliipatia halmashauri hiyo shilingi bilioni 1.8 kwa ajili ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri. Vilevile, mwezi Februari, mwaka 2021 Serikali iliipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 500 kwa ajili ya ujenzi wa wodi tati katika Hospitali ya Halmashauri na imetenga shilingi milioni 500 katika bajeti ya mwaka 2020/2021 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba katika hospitali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwezi Februari, 2021, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Busega shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati za Ng’wang’wenge, Sanga na Mkula. Vilevile, katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, Serikali imetenga shilingi milioni 150 kwa ajili ya kukamilisha maboma ya Zahanati ya Imalamate, Ijutu na Busami katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kuimarisha miundombinu ya huduma za afya katika Jimbo la Busega na nchini kote ili kuendelea kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza:-

Je, ni lini Mradi mkubwa wa Maji wa Ziwa Victoria kutoka Busega mpaka Itilima kupitia Bariadi utaanza kutekelezwa?
NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songwe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la KFW la Serikali ya Ujerumani imekamilisha taratibu za kupatikana kwa wataalam washauri ambao watasimamia utekelezaji wa mradi huu mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria kupeleka Mkoa wa Simiyu. Mradi huu unahusisha ujenzi wa bomba kuu kilomita 195, matenki 8 yenye ujazo wa lita milioni 11.9 na mabomba ya usambazaji kilomita 49.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa mradi unatarajia kuanza mwezi Agosti 2021 na miji mikuu ya Wilaya itakayonufaika ni Busega, Bariadi, Itilima, Maswa, Meatu na vijiji vilivyoko pembezoni mwa bomba kuu umbali wa kilomita 12 kila upande. Mradi umepangwa kutekelezwa kwa miaka minne.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kutoka Nyashimo Wilayani Busega hadi Dutwa Wilayani Bariadi kupitia Shigala, Malili, Ngasamo na Imakanate yenye kilometa 47 kwa kiwango cha lami?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Nyashimo –Dutwa ni barabara ya Mkoa yenye ureu wa kilometa 47 inayohudumiwa na Wizara yangu kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS).

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Nyashimo –Dutwa ipo katika mpango mkakati wa Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi (Ujenzi) kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS) wa mwaka 2021/2022 – 2025/2026 kwa ajili ya kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina. Barabara hii inaendelea kufanyiwa matengenezo mbalimbali pamoja na ujenzi wa madaraja ili iweze kupitika majira yote ya mwaka ambapo katika mwaka wa fedha 2021/2022 imetengewa shilingi milioni 1,102.607 kwa ajili ya matengenezo pamoja na ujenzi wa Daraja la Shigala na la Malili. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatoa kipaumbele kwa Wilaya ya Busega kujengewa Mahakama ya Wilaya ili kuondoa usumbufu ambao wananchi wanaupata kwa kusafiri hadi Wilaya ya Bariadi kufuata huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Katiba na Sheria, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa Mahakama ya Busega ni moja ya miradi itakayojengwa katika Mwaka wa Fedha 2021/2022. Mkandarasi wa ujenzi wa Mahakama hii amepatikana ambaye ni United Builders na kukabidhiwa eneo la ujenzi mwezi Oktoba. Kazi za ujenzi zimeanza na zinatarajiwa kukamilika ifikapo Aprili, 2022.

Mheshimiwa Spika, Mahakama ya Tanzania inaendelea kutekeleza programu ya maboresho ya majengo ya Mahakama zake na kukarabati majengo ya Mahakama katika ngazi mbalimbali za Mahakama hapa nchini ili kusogeza huduma karibu na wananchi na kuboresha mazingira ya kazi. Ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Barabara ya kutoka Igalukilo - Sayaka inayounganisha Mikoa ya Mwanza na Simiyu itahamishiwa TANROADS?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Barabara, Namba 13 ya mwaka 2007 na Kanuni zake za mwaka 2009, imeainisha vigezo na utaratibu wa kuhamisha barabara ili iwe chini ya TANROADS ambapo barabara inaweza kupandishwa au kuteremshwa toka daraja moja kwenda daraja lingine.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaielekeza Halmashauri ya Wilaya Busega kupitia TARURA kufuata utaratibu huo ili kuiweka barabara hiyo katika mpango wa kupandishwa hadhi na kuwa ya mkoa.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha Kituo cha Afya Kiloleli pamoja na kupeleka Vifaa kwenye Hospitali ya Wilaya Busega?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu: -

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya Kiloleli kilipandishwa hadhi kutoka Zahanati kuwa Kituo cha Afya mwaka 2016. Serikali imeendelea kuboresha miundombinu ya Kituo hicho ambapo jumla ya shilingi milioni 57 zilipelekwa katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya kujenga Wodi ya Wazazi na ujenzi wa Jengo la stoo ya dawa. Aidha, katika mwaka wa fedha 2021/2022 shilingi milioni 90 zimepelekwa kwa ajili ya ujenzi wa nyumba ya watumishi, kwa maana ya three in one, ujenzi ambao upo katika hatua ya msingi. Mpango wa Serikali ni kuendelea kutenga fedha kwa awamu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imetenga shilingi milioni 500 katika mwaka wa fedha 2021/2022 kwa ajili ya unununuzi wa vifaa tiba kupitia Bohari Kuu ya Dawa. Tayari baadhi ya vifaa tiba vimeshapelekwa kwenye Hospitali ya Halmashauri ya Busega. Ahsante sana.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Chuo cha VETA katika Halmashauri ya Wilaya ya Busega?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu Sayansi na Teknolojia naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni azma ya Serikali kujenga Chuo cha Ufundi Stadi katika kila Mkoa na Wilaya nchini. Katika mwaka wa fedha 2022/2023, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 100 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa vyuo vya VETA katika Wilaya 63 ambazo hazina vyuo hivyo, kiasi hiki pia kitatumika katika ujenzi wa Chuo cha VETA cha Mkoa wa Songwe. Busega ni miongoni mwa Wilaya 63 ambazo zipo kwenye mpango wa kujengewa Vyuo vya Ufundi Stadi katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali imeshakamilisha maandalizi ya awali ikiwemo upatikanaji wa maeneo kwa ajili ya ujenzi pamoja na kuandaa michoro na makadirio ya gharama za ujenzi kwa kila chuo na ujenzi huo unatarajiwa kuanza mara tu taratibu za manunuzi zitakapokamilika, nakushukuru sana.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri haya majibu yanataja Mkoa wa Songwe na lile lililopita pia Mkoa wa Songwe una kitu special huu Mkoa wa Songwe?

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, katika mikoa 26 ya Tanzania Bara ni Mkoa wa Songwe peke yake ndio ambao haujajengewa Chuo cha VETA cha mkoa. Kwa hiyo ni lazima tuutaje kwa sababu ni mkoa pekee ambao hauna na katika mwaka huu wa fedha tumeuweka kwenye mpango na tutakwenda kujenga katika Mkoa wa Songwe. (Makofi)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza:-

Je, lini Serikali itajenga Wodi ya Akinamama, Watoto na Wanaume katika Vituo vya Afya Lukungu - Lamadi na Kiloleli?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Vituo vya Afya vya Lukungu na Kiloleli ni miongoni mwa vituo vilivyosajiliwa na kuanza kutoa huduma vikiwa na upungufu wa miundombinu ikiwemo Wodi ya Wazazi, Jengo la Upasuaji na Maabara.

Mheshimiwa Spika, Serikali itaendelea kutenga bajeti kwa awamu kwa ajili ya ukarabati na upanuzi wa miundombinu inayopungua kwenye vituo vya afya kote nchini vikiwemo Vituo vya Afya vya Lukungu na Kiloleli, ahsante.
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE aliuliza: -

Je ni lini ahadi ya Rais wa Awamu ya Tano ya kuipandisha hadhi Shule ya Sekondari Nassa itatekelezwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu Swali la Mheshimiwa Simon Songe Lusengekile, Mbunge wa Jimbo la Busega, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia Mwongozo wa Uanzishaji na Usajili wa Shule wa Mwaka 2020 uliotolewa na Wizara ya Elimu unabainisha hatua za kuipandisha hadhi shule kuwa ya Kidato cha Tano na Sita kama ifuatavyo: -

Mwombaji ambae ni Mkurugenzi ataandika barua kwa Kamishna wa Elimu kupitia Mdhibiti Mkuu wa Ubora wa Shule Kanda. Barua hiyo itaambatishwa na taarifa ya ukaguzi wa Mdhibiti wa Ubora wa Shule Kanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumuagiza Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Busega kutenga fedha kupitia mapato ya ndani ili kukamilisha miundombinu muhimu inayowezesha shule hii kukidhi vigezo vya kupandishwa hadhi ya kuwa na Kidato cha Tano na cha Sita.