Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Simon Songe Lusengekile (21 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nianze kwa kukushukuru kwa kunipa nafasi kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais. Pia nimshukuru Mungu sana kwa nafasi hii aliyotupatia ya kuwa mahali hapa leo. Kipekee nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi pamoja na wananchi wa Jimbo letu la Busega kwa kuniamini na kunichagua kuwa mwakilishi wao mahali hapa.

Mheshimiwa Spika, 2015 nilibahatika kufuatilia hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati akizindua Bunge la Kumi na Moja, tarehe 20 Novemba, 2015. Aliyoyasema nilianza kufikiri kwamba yanaenda kuwezekana vipi, lakini nirudishe shukrani nyingi sana kwa mapinduzi makubwa ya maendeleo aliyotupatia Mheshimiwa Rais kwa kipindi hiki cha miaka mitano iliyopita. Ni Imani yangu kubwa kwamba katika hii miaka mitano kupitia hotuba yake ya tarehe 13 Novemba, 2020 ambayo ilitoa mwelekeo wa nchi yetu yapo maeneo machache naomba nami nichangie.

Mheshimiwa Spika, kuna suala toka asubuhi linaendelea kujadiliwa; habari ya TARURA. TARURA ni pasua kichwa, TARURA ni shida mpaka sasa barabara nyingi vijijini zimekatika. Pia kutokuwepo kwa barabara hizi za vijijini kumesababisha sehemu ya uchumi wa wananchi wetu kushuka kwa sababu hawawezi sasa kupeleka hata mazao yao kwenda kutafuta sehemu ambako kuna masoko, madalali wamekuwa wengi wa bei ya chini kwa sababu ya shida ya barabara ambazo ziko kwenye vijiji ambavyo sisi tunatoka.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano ukiangalia kuna wakati hata hili zao la pamba kwetu kule Usukumani ambapo wananchi wengi wanalima, inafikia sehemu barabara ni ya shida watu wa pikipiki wanakwenda kununua pamba kwa bei ya chini sana, muda mwingine hata nusu ya bei ambayo ni halisia kwa sababu ya kutokuwepo barabara sehemu husika. Tunapotaka sasa kuendeleza uchumi wa wananchi wetu mmoja mmoja lazima tuwatengenezee mazingira mazuri ili wananchi hawa sasa waweze kusafirisha mazao yao ya biashara kwenda sehemu nyingine kwa ajili ya kupata bei iliyo salama.

Mheshimiwa Spika, nataka pia nichangie kidogo eneo la kilimo. Mimi ni muumini sana wa uwekezaji katika sekta ambazo ni productive kwa nchi yetu. Tunapokuwa tunazungumza habari ya ajira milioni nane, ni lazima tufikiri kuelekeza baadhi ya ajira katika sehemu ambazo ni productive kwa nchi yetu ikiwemo na kilimo.

Mheshimiwa Spika, ukienda kwenye halmashauri zetu, halmashauri zilizo nyingi zina shida ya watumishi, hasa Maafisa Ugani. Wananchi wetu wengi hawapati fursa ya kufundishwa na hawa Maafisa Ugani kwa sababu hawapo kila sehemu ni shida. Hii ni sekta ambayo tungeweza kuielekezea watumishi wengi wangeweza kuwasaidia wananchi wetu ambao wanalima kwa kutumia akili zao zilezile ambazo Mheshimiwa Mbunge wa Mbogwe alikuwa anajaribu kugusia.

Kwa hiyo, mimi niseme na niombe, tunapokuwa tunaangalia suala la ajira, lazima pia tuangalie eneo hili ili tuweze kuajiri watu wengi waende wakawasaidie wananchi wetu katika suala zima la kilimo na kilimo kiwe chenye tija na tutakapopata malighafi yetu basi itatumika kwa ajili ya viwanda vyetu vya ndani.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka kulizungumzia ni viwanda. Eneo hili tukitaka tufanye vizuri ni lazima tuhakikishe kwamba tunapata viwanda vyetu vya ndani ambavyo vinatengeneza bidhaa mpaka mwisho. Kama ni pamba basi tutengeneze bidhaa inayotokana na pamba mpaka mwisho tupate nguo ili tuweze ku-export nguo kwenda nje ya nchi, zao ambalo tayari limekamilika kwa kutumia bidhaa zetu za ndani.

Mheshimiwa Spika, pia nataka kuongelea habari ya uvuvi, Mbunge wa Ukerewe amezungumza kidogo. Eneo hili bado lina shida, tozo ni nyingi sana kwa wananchi wetu ambao wanashughulika katika suala zima la uvuvi. Tozo ni nyingi, kuna leseni ya mtumbwi, TASAC Sh.70,000 wananchi wetu wanalipa lakini pia kuna leseni za halmashauri, kuna leseni ya mtumbwi na kuna shilingi 20,000 leseni ya mvuvi mmoja mmoja. Haya maeneo wananchi wetu wanayalalamikia sana kwa sababu tozo zimekuwa nyingi na wanashindwa kuzimudu kutokana na hali ya uchumi ambao wanao. Kwa hiyo, niombe Wizara husika waje na mpango kuona namna ya kupunguza baadhi ya tozo kwa hawa watu wetu ambao ni wavuvi ili waweze kunufaika na kazi ya uvuvi ambayo wanafanya.

Mheshimiwa Spika, nizungumzie sekta ya afya. Eneo hili asubuhi limechangiwa katika hoja mbalimbali kupitia maswali. Huduma ya bila malipo kwa akina mama wajawazito, watoto na hata wazee; ni kweli kuna baadhi ya hospitali zinatoa lakini kuna shida kubwa sana ya upatikanaji wa dawa katika sehemu ambazo wananchi hawa wanatibiwa. Ama dawa MSD hazipatikani lakini hata kama zikipatikana basi mpango mzima wa kando unafanyika na kunakuwa na shortage kubwa sana ya dawa.

Mheshimiwa Spika, tumeona hata Mheshimiwa Waziri wa Afya amejaribu kwenda na hoja ya kutaka kuangalia equation tu iliyopo kati ya uwepo wa panadol na mwananchi kukosa dawa na akasema hii siyo simultaneous. Mimi nimpongeze kwa namna ya pekee sana kwa jinsi ambavyo ameamua kuja kwa kasi na kuhakikisha kwamba sehemu zetu dawa zinaendelea kuwepo na wananchi wetu wanapata dawa.

Mheshimiwa Spika, niombe sasa, MSD bado kuna shida. Tunaweza kwenda na order kubwa ya dawa na fedha ambazo tayari ziko MSD lakini MSD inakosa dawa. Niombe sasa Serikali kupitia Wizara ya Afya kuhakikisha kwamba tunaimarisha MSD ili iweze kuwa na sehemu kubwa ya kupata dawa ili wananchi wetu sasa waweze kupata dawa katika sehemu ambazo wanakuwepo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nilitaka kuchangia ni maliasili na utalii. Kuna shida kubwa sana ya tembo kusumbua na kuharibu mazao ya wananchi wetu. Nizungumzie kwa mfano kule kwangu Jimboni Busega kuna Kata za Lamadi, Mkula kwa maana ya Kijereshi, kuna shida kubwa ya tembo. Katika mwaka uliopita 2020, zaidi ya wananchi wanne wameuawa na tembo kwa sababu ya kukaa katika kata hizo ambazo nimeweza kuzitaja.

Mheshimiwa Spika, kuna haja kubwa sana ya kuimarisha ulinzi wa wanyamapori kupitia maaskari wetu. Ninajua Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofika pale kwenye jimbo langu aliahidi kutupatia askari 26 ili waongeze kuimarisha ulinzi wa wanyamapori na hii itatusaidia sana wananchi wetu kufanya kazi zao wakiwa na amani. Sasa kwa sababu mazao yao yanaharibiwa tunawapa tena wakati mgumu wa kupata mazao ili waweze kunufaika na mazao yao.

Mheshimiwa Spika, naomba sasa kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kutuwezesha kuwa hapa. Lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa nchi yetu. Nimpongeze pia Mheshimiwa Vuma kwa kuitambua na kukubali mafanikio ya Timu ya Simba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite katika mambo machache sana kuchangia mpango huu ili kuendelea kuimarisha uchumi wetu. Lakini ijulikane ya kwamba ni lazima sisi kama Wabunge tuendelee kuisimamia Serikali ili tufikie ule mpango ambao unasemwa sasa wa per capita income dola 1,400 katika hii miaka mitano ijayo. Kwasababu sasa ni 1,080 na cut off ni 1,036. Kwa hiyo, bado tuko katika eneo ambalo si salama kwa sababu tofauti yake ni dola 44. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Nchi ya Algeria mwaka 2019 per capita income ilikuwa 4,060 lakini 2020 ilishuka ikawa 3,970. Kwa hiyo, kushuka pia inawezekana. Kwa hiyo, sisi kama Wabunge lazima tuisimamie Serikali ili uchumi wetu uendelee kupanda kama ambavyo Mheshimiwa Waziri wa Fedha ameeleza katika mambo matano ambayo ameyazungumza yatakayokwenda ku-reflect uchumi wetu. Na ninaomba uchumi huu sasa uende uka-reflect kwa wananchi hawa waliopo huko kwenye majimbo yetu na wananchi kwa ujumla wa nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi watu wa Simiyu ukitafuta identity yetu ni zao la pamba. Lakini wananchi wetu wameshapoteza hope na zao la pamba. Kwa nini; kwasababu ya bei ya zao la pamba. Leo ninataka kuzungumza kidogo kuiomba Serikali kutafuta namna ya kuwezesha Mkoa wa Simiyu kuupelekea kiwanda, hasa cha kuzalisha vifaa tiba vitokanavyo na zao la pamba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tukipata kiwanda hiki maana yake zao la pamba sasa bei yake itaenda kuimarika. Na zao la pamba likiimarika maana yake sasa tutarudisha morali ya wananchi wetu kulipenda na kulima tena zao la pamba ambalo litaongeza uchumi wa wananchi wetu walioko huko kwenye Mkoa wa Simiyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kiwanda hiki kitasaidia nchi yetu kwa namna ya pekee sana kwasababu kitazalisha zaidi ya ajira ambazo ni rasmi 600 na ajira ambazo si za moja kwa moja zaidi ya 1,000. Wananchi watapata ajira, watalipa kodi, watapata kipato, na hii sasa itakwenda kuimarisha uchumi wa nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niombe Wizara ya Uwekezaji iendelee kuhakikisha kwamba inawekeza kiwanda hiki katika Mkoa wa Simiyu ili zao la pamba, kama nilivyosema pale awali, liweze kuimarika.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukitengeneza vifaa tiba vitokanavyo na pamba maana yake tunakwenda sasa kuimarisha kutokuagiza vifaa hivi nje zaidi ya asilimia 38.3. Asubuhi tumesikia hapa, tunaagiza zaidi ya asilimia 80. Sasa tukiwekeza kwenye kiwanda hiki tunakwenda kupunguza uagizaji kwa asilimia zaidi ya 38.3 ambapo tunatumia zaidi ya bilioni 147 kila mwaka kuagiza vifaa tiba nje ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni imani yangu kwamba Waziri wa Fedha, Mawaziri wanaohusika, mtatusaidia kuhakikisha kwamba tunapata kiwanda kule Mkoa wetu wa Simiyu ili tuweze kuzalisha vifaa tiba vikiwemo cotton gauze, cotton swab na nguo za madaktari na manesi pamoja na mashuka ambayo yanaweza kutumika katika hospitali zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niombe Wizara ipunguze tozo mbalimbali kwa ajili ya wawekezaji. Lakini pia mamlaka husika ziwe na lugha moja, hasa mamlaka zinazotoa vibali kwa hawa wanaokwenda kuwekeza kwenye miji yetu. Nilitaka nizungumzie sana hapo kwenye eneo la kilimo ili wananchi wetu sasa wakanufaike. (Makofi)

Kwenye eneo la kilimo bado hatujawekeza mahususi katika kilimo cha umwagiliaji. Bado hatujatumia Ziwa letu Victoria, hasa kwenye Mwambao wa Ziwa Victoria, bado hatujalitumia vizuri katika suala zima la kilimo cha umwagiliaji. Ukianzia kule Rorya, ukija Musoma, ukija Bunda, ukija pale Busega, ukienda Magu, Mwanza, Sengerema, Buschosa na huko mpaka Bukoba, bado hatujatumia ziwa letu katika kilimo cha umwagiliaji. Kwa hiyo, niombe Wizara ya Maji ijikite kuhakikisha kwamba tunaimarisha miundombinu ili tuwe na kilimo cha umwagiliaji katika sehemu zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapongeza mradi ulioko mkubwa wa kuleta maji hapa; mzuri sana. Lakini pia niseme sisi ambao tunazungukwa na Ziwa Victoria bado tuna shida kubwa ya maji. Mfano kwenye Wilaya ya Busega wanaotumia maji safi na salama ni asilimia 42.9; bado tatizo ni kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tunapokuwa tunaangalia suala hili la maji pia tuone kabisa kwamba linaenda ku-reflect kilimo cha umwagiliaji kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ambalo nataka kuchangia hapa ni eneo la asilimia10 ambazo zimepangwa kisera kwenye halmashauri zetu, ambapo asilimia nne ni kwaajili ya vijana, asilimia nne kwaajili ya akina mama na asilimia mbili kwaajili ya walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ipo kisheria na imepangwa lakini cha kusikitisha ni kwamba haifuatwi na hakuna anayefuatilia. Unakuta Halmashauri imepata mapato ya ndani safi lakini asilimia ambazo zinaenda kwenye group hili hazifiki hata 10, na hamna anayehoji wala anayesimamia. Wakurugenzi hawaojiwi, business as usual.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili lazima tulisimamie. Kama ni asilimia 10 itengwe kweli, kama makusanyo ya ndani ni bilioni moja asilimia 10 ni milioni 100, no discussion kwenye hili, ipelekwe milioni 100 sehemu husika. Lakini sasa hivi inaweza ikawa milioni 100 zikaenda milioni tano, milioni saba, hamna anayehoji, hamna anayechukua hatua, ni lazima eneo hili twende tukachukue hatua ili sasa vijana wetu tuwaimarishe na waweze kupata fedha hizi ili sasa waweze kuzitumia katika kuinua kipato chao pamoja na hawa akina mama na watu wenye ulemavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichangie kidogo kwenye eneo la maliasili na utalii. Nimesikia kengele ya kwanza. Ukitoka Lamadi kuelekea Bunda pale katikati ya Lamadi na Bunda kuna wanyama wa Mbuga ya Serengeti. Ningeishauri Serikali, ili kuinua pia uchumi wa maeneo yale tufungue namna ya wanyama wetu waweze kwenda hadi ziwani, ukienda pale Nyatwali wanyama waende mpaka ziwani. Nasema hivi kwasababu itafungua uwekezaji katika Miji yetu ya Lamadi na Bunda na wananchi wa pale watazidi kunafaika na hali halisi ya uwekezaji ambao utapatikana maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya Maliasili iliangalie hili, ni eneo mojawapo ambalo tunaweza kuwekeza na ni eneo mojawapo ambalo linaweza kuipatia fedha Serikali, na hasa hasa katika hizi sehemu ambazo nimezitaja ikiwemo na mji wa Lamadi ambao sasa ni mji mkubwa, pamoja na mji mwingine wa Bunda. Eneo hili lazima tulitazame ili liweze kuingiza kipato katika eneo letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie kidogo habari ya TARURA, TARURA lazima tuitafutie fedha; kama TANROADS wanapata asilimia 70 na TARURA asilimia 30 kuna haja ya kuzungumza hapa tena. Kuna haja ya kuendelea kuingalia TARURA kwa jicho la pili, kuna haja ya kuingozea fedha ili maeneo yetu sasa yatengenezwe. Kule vijijini na kwenye majimbo tatizo la TARURA ni kubwa, tatizo la TARURA linalalamikiwa kila mahali. Barabara hazipitikim ukienda pale jimboni kwangu barabara ya kutoka Mwamanyiri kwenda Badugu haipiki, barabara nyingi hazipitiki. Sasa hata kama wazalishaji wa pamba watazalisha hatimaye tutazungumza tena habari ya barabara. Kwamba sasa gari zinaendaje kuchukua pamba huko ambako pamba imezalishwa kuja hapa mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapokuwa tunazungumzia kuimarisha uchumi wa watu na kuimarisha uchumi wa mtu mmoja mmoja lazima pia tuziangalie bajeti ya TARURA.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe Wizara ya TAMISEMI, lazima tuje tuzungumze, na hapa lazima tuje tuone hali halisi ya namna ya kuiwezesha TARURA ili iweze kufanya kazi kubwa kwa ajili ya wananchi wetu. Wapo wengine ambao wamekuwa wakisema irudi TANROAD, Wizara ya Ujenzi lakini hapa issue sio kurudi TANROAD issue ni kuiongezea fedha ili iweze kufanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja na kazi iendelee. (Makofi).
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia taarifa za Kamati zetu tatu, PAC, LAAC pamoja na PIC. Kwanza nianze kwa kuzipongeza sana Kamati hizi tatu kwa kazi kubwa ambazo wamefanya kuhakikisha kwamba wanapata ripoti iliyo salama na wametuletea hapa leo.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya ya kutafuta fedha, ingawa yapo mambo ambayo yameelezwa kwenye taarifa za Kamati ambayo si mazuri kwa nchi juu ya ubadhirifu wa fedha za Serikali.

Mheshimiwa Spika, katika ripoti hii nitajikita maeneo matatu. Jambo la kwanza ni eneo la Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Pia nitachangia uendeshwaji wa Kiwanja cha Ndege Kilimanjaro (KIA) na la tatu kama muda utakuwa bado unaruhusu nitazungumza kidogo Wakala wa Mabasi Yaendayo kwa Haraka (DART).

Mheshimiwa Spika, CAG amefanya ukaguzi wa ufanisi katika Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Kuna mambo yamebainika ambayo yanahitaji kupelekewa miongozo ya namna ya uendeshaji wa mifumo ya upatikanaji wa wanafunzi ili waweze kunufaika na mikopo inayotolewa.

Mheshimiwa Spika, jana tumezungumza sana hapa juu ya hoja ambayo ililetwa na Mheshimiwa Ezra juu ya wanafunzi ambao hawajapata mikopo. Katika ukaguzi huu wa ufanisi uliolenga kuangalia ufanisi wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wetu. Vilevile ukaguzi huu ulilenga kuangalia ufanisi wa namna zinavyoshughulikiwa rufaa pale ambapo wanafunzi wanapokuwa wamekata rufaa juu ya upatikanaji wa mikopo yao.

Mheshimiwa Spika, yapo mambo machache ambayo yamebainika. Kwenye taarifa ile alifanya ukaguzi wa miaka mitano, lakini kuna mwaka 2018/2019 mwaka ule ulikuwa na shida kubwa. Ilibainika kwamba wanafunzi 6,182 walipewa mikopo zaidi ya kiwango walichotakiwa kupewa chenye thamani ya 5,670,000,000, kiwango hiki kama wangepewa wanafunzi wengine ambao hawakupata mikopo tungepata wanafunzi wengine 2,835. Tungegawa katika halmashauri zetu 184, kila halmashauri wanafunzi 15 wangenufaika na fedha hizi ambazo walipewa wanafunzi zaidi ya kile walichokuwa wanahitaji.

Mheshimiwa Spika, nikisema hivi naamanisha nini hapa? Namaanisha kwamba mwanafunzi amekubaliwa kupewa kiasi fulani cha mkopo, lakini katika reality wakati anapokuja kupewa mkopo ule anapewa zaidi ya kile kiwango alichokubaliwa, inapelekea wanafunzi wengine kukosa mikopo na huu ulikuwa ni mwaka mmoja wa 2018/2019. Ukiangalia katika miaka yote mitano aliyofanya ukaguzi wa ufanisi CAG 13,000,000,000 zilizidishwa kwa wanafunzi ambao walikuwa wanapewa zaidi ya mikopo husika.

Mheshimiwa Spika, wanafunzi 2,852 walipewa mikopo chini ya kile kiwango walichokuwa wamekubaliwa pale awali. Hii inaamanisha nini? Maana yake mwanafunzi amekubaliwa atapewa asilimia kadhaa, lakini mwisho wa siku anakuja kupewa chini ya kile kiwango ambacho alitakiwa kupewa. Tunamfanya mwanafunzi asimalize masomo yake au tunamfanya mwanafunzi kuhangaika na masomo yake. Nini kilifanyika hapa? Zaidi ya 1,147,000,000 wanafunzi hawakupewa stahiki waliokuwa wanatakiwa kupewa.

Mheshimiwa Spika, wanafunzi 756 walipewa mikopo bila kuwa na sifa za kupewa mikopo, yaani hawana sifa ya kupewa mikopo lakini wakapewa, thamani yake 2,255,000,000. Hapa napo tungepata wanafunzi wengi ambao wangeweza kunufaika na mikopo hii hata pale Mbeya Jiji nao wangepata kupitia fedha ambazo kuna wanafunzi walipewa ambao walikuwa hawahitajiki kupewa mkopo.

Mheshimiwa Spika, nini sasa hapa tafsiri yake? Tafsiri yake katika Bodi yetu ya Mikopo bado kuna shida ya mfumo unaotumika katika utoaji wa mikopo ya elimu ya juu. Kama mwanafunzi alitakiwa kupewa 1,000,000 anapewa 1,200,000 tafsiri yake ufanisi wa ule mfumo siyo salama. Hapa umefanyika ukaguzi wa ufanisi. Sasa ukifanyika ukaguzi wa hesabu itakuwa tatizo zaidi.

Mheshimiwa Spika, nashauri sasa kama inawezekana tufanye ukaguzi wa kina juu ya mfumo unaotumika wa utoaji wa mikopo kwa wanafunzi wa elimu ya juu. Ukisoma ripoti ya CAG inakupa indication kwamba mfumo siyo salama kwa kutoa mikopo kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile katika ukaguzi huu uangalie hizi 5,670,000,000 za 2018/2019 walipopewa wale wanafunzi zaidi hao wanafunzi walikuwepo kule site au kuna watu walikuwa wanawapa halafu baadaye wanakwenda kuzichukua? Hizo ndio indication za hii. Je, hao wanafunzi waliopewa mkopo wakati hawana sifa hao waliowapa bado wako ofisini? Kwa hiyo ukifanyika ukaguzi wa kina utayabaini haya mambo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende eneo la pili, eneo la uendeshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro unaoendeshwa na Kampuni ya KADCO, hapa bado kuna shida. Kampuni ya KADCO iliingia mkataba na Serikali mwaka 1998 ili kuendesha Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro kwa miaka 25. Wakasainishana mkataba, ule mkataba Serikali ikawa na hisa asilimia 24 na kampuni ikawa na hisa asilimia 76. Katika kuendesha ule uwanja inaonekana ufanisi haukuwa mzuri. Serikali 2009 kupitia Baraza la Mawaziri wakakubaliana kununua hisa zote za KADCO kwa asilimia 100. Mwaka 2010 Serikali ilinunua hisa zote za KADCO kwa asilimia 100. TAA ililipa fedha milioni 5.3 fedha za Kimarekani sawa na milioni karibu 12.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2010 baada ya Serikali kununua zile hisa nini kiliendelea? Uendeshwaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro umeendelea kuendeshwa kama private entity. Wameendelea kuwa na mkataba wa concession agreement. Sasa unajiuliza maswali ya kutosha. Swali la kwanza, kama Serikali imenunua hisa zote asilimia 10,0 maana yake Serikali 100% ndio mmiliki wa kiwanja. Kwa tafsiri ya kawaida uendeshwaji wa kiwanja ulitakiwa kuwa chini ya Serikali kupitia TAA. Sasa hii concession agreement iliyopo wanaoendelea kutumia mpaka leo mpaka kesho na jana ni kati ya mkataba wa Serikali na watumishi wa KADCO walioko Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro au ni kati ya KADCO kama private entity na Serikali? Kama ni hili la pili nini maana ya kununua hisa kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama Baraza la Mawaziri lilishauri kiwanja kile kiendeshwe na TAA kwa nini hakikuendeshwa mpaka leo? Kwanza cha ajabu zaidi hata fedha wanazokusanya KADCO mpaka leo tunaweza kusema wanazitumia fedha mbichi, kwa nini? Kwa sababu hazipiti Mfuko Mkuu wa Serikali, yaani wao wanakusanya kesho wanapanga matumizi, wanatumia. Wana kipengele kidogo tu wanalipa dividend Serikalini kwa TR hapo tu. Mwaka 2021wame-declare kulipa 350,000,000.

Mheshimiwa Spika, sasa nashauri kwamba, kwa kuwa Serikali ilinunua hisa zote asilimia 100, sasa kiwanja hiki shughuli zote za uendeshaji zirudi TAA. Kwa nini nasema hivyo? tulipohoji kwa Afisa Masuhuli kwa nini wameamua kuendeleza hizi alitujibu jibu simple sana anasema kiwanja hiki kipo kimikakati ya kibiashara. Sasa mimi tu wa la saba wa Busega kule inaniingia kweli kichwani kwamba Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaam hakiko kibiashara eti cha Kilimanjaro kiwe kibiashara zaidi? Kama ingekuwa ni kibiashara basi Kiwanja cha Ndege cha Dar es Salaam ndicho kiko kibiashara zaidi kuliko Kiwanja cha Kilimanjaro. Kwa hiyo, nashauri tufanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili tufanye special audit ili kuangalia mapato yote yaliyopatikana katika miaka 10 hii yote ambapo KADCO walikuwa wanaendesha kiwanja kile kama Serikali, ili tubaini kama fedha hizi zilitumiwa vizuri na sheria za fedha zilifuatwa. Tukifanya yale yote yatatusaidia kujua ni kwa kiwango gani tumepata hasara kule Kilimanjaro. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine ambacho nataka nichangie ni Wakala wa Mabasi Yaendayo kwa Haraka (DART). Tumeona Taarifa ya Kamati imesema hawa DART walilipa 1,700,000,000 kama fidia kwa wananchi kuachia maeneo, lakini CAG anasema fedha hizi zilikuwa nyongeza ya malipo nje ya valuation report iliyokuwepo, yaani Valuation inasema lipa 5,000,000,000 wao wakalipa zaidi 1,700,000,000. Sio hivyo tu, wakalipa na posho za usumbufu 435,000,000. CAG alipoomba kibali, walipata wapi kibali cha kuongeza kulipa fidia hawana. Hivi kweli wanapata wapi ujasiri wa kulipa 1,500,000,000 nje ya valuation report? Wanajibu kirahisi tu waliambiwa na Serikali. CAG anauliza leteni hicho kibali mlichopewa na Serikali, hawana. Hivi tumefika kuendesha taasisi yetu kwa style hiyo?

Mheshimiwa Spika, hapa kuna madudu ya kutosha juu ya malipo ya 1,500,000,000. Vilevile hapa tufanye special audit kuwabaini wale wote waliolipwa 1,500,000,000 kama ilikuwa ni halali. Pia wachukuliwe hatua watumishi ambao wameisababishia hasara Serikali kwa kulipa watu bila kufuata valuation report.

Mheshimiwa Spika, fedha hizi ni fedha za Watanzania na kibaya zaidi miongozo inasema valuation ikifanyika leo baada ya miezi sita, mnaongeza interest kwa wale mliowakadiria. Baada ya miaka miwili, miongozo inasema kurudia valuation. Sasa wale muda umepita miaka 10, hawajafanya tena valuation, wanaibuka tu kulipa zaidi 1,570,000,000. Hili haliwezekani tufanye special audit DART ili tupate taarifa rasmi, fedha hizi wahusika waliolipwa na tuone tija kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo moja la kumalizia. Ukienda pale Soko la Kariakoo, nafikiri liliungua mwezi Julai mwaka jana, pale napo kuna shida. Tunawaza kwamba, baada ya kufunga mwaka wa fedha 2021 kwa maana Juni, baada ya siku 10 tu soko likaungua, documents zote zikaungua, hamna cha risiti ya mapato, hamna cha risiti ya matumizi. CAG amewapa unqualified report, lakini ni kwa nini? Hapana siyo unqualified report amewapa disclaimer report ameshindwa kutoa maoni kwa sababu hamna document yoyote inayomfanya ku-verify mapato ya 3, 500,000,000 na matumizi ya 3,500,000,000.

Mheshimiwa Spika, sasa hii kwa akili tu ya kawaida inanitafakarisha na kunifanya nione inawezekana Soko la Kariakoo liliungua baada ya documents hizi kutoonekana ofisini. Ni akili tu ya kawaida inanituma hivyo. Kwa nini baada tu ya kufunga mwaka wa fedha Juni, siku 10 tu, halafu mwisho wa siku CAG ameenda pale hamna document yoyote ameshindwa ku-verify matumizi ya 3, 500,000,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa leo nimekuja na special audit tu mwanzo mwisho. Hapa napo ifanyike special audit ya 3,500,000,000 tujue tatizo kubwa lilikuwa ni nini. Sasa sijui watapata wapi document, lakini najua kwa sababu itakuwa ni special na kwa sababu special unaweza ukawahoji watu, CAG atajua namna ya kufanya, lakini mwisho wa siku tupate mbichi na nzuri kwa hapa kwenye Soko la Kariakoo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja za Kamati. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia Wizara ya Maji. Kipekee sana nimpongeze sana rafiki yangu Mheshimiwa Aweso kwa kazi kubwa anayofanya pamoja na Naibu Waziri na Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji. Wanafanya kazi kubwa, tunaona kazi zao wanazofanya, kweli zimekuwa ni kazi za msingi. Niwaambie tu kwamba wananchi hasa wananchi wa Busega wana imani kubwa nao kwa sababu wameona mageuzi makubwa ambayo wameyafanya kwenye Wizara ya Maji kwa huo muda mfupi ambao wamekuwa kwenye madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mageuze hayo ni Pamoja na namna ambayo wamefanya kuhakikisha kwamba wanapunguza gharama za ujenzi wa miundombinu ya maji, kwa sababu tumeona kuna sehemu zingine ambazo wameenda, gharama zimeshuka, unakuta BOQ ilikuwa bilioni mbili lakini kwa sababu wamenda pale mmefanya revision ya budget zimeshuka mpaka kufikia hata bilioni 1.6. Haya ni mageuzi makubwa sana ya kimkakati ambayo wameamua kuyafanya kwenye Wizara yenu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kipekee pia nimshukuru sana Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa alipokuja pale kwangu Mkura aliahidi kutupatia mradi wa maji na sasa mradi tayari umeshaanza kazi, tayari wakandarasi wako pale wanafanya kazi. Kwa kweli, tunawapongeza sana na muda ujao naamini kwamba mradi huu utaanza kutoa maji. Nimwombe tu rafiki yangu Waziri, bado kuna shida ya fedha pale. Naomba apeleke fedha ili mradi ule ukamilike kwa wakati na naamini kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri ni msikivu na kwa sababu ni kijana na kwa sababu Wasukuma ni wakarimu aende pale akaangalie namna mradi unavyotekelezwa ili umalizike kwa haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumze suala moja ambalo limekuwa likinipa shida kidogo. Kuna baadhi ya miradi ambayo inaenda kutelekezwa kwenye kata, lakini unakuta kata moja ina vijiji vine, lakini mradi unakuwa wa vijiji vitatu, kijiji kimoja kinabaki. Hili limekuwa ni tatizo na niishauri Wizara, kama wameamua kupeleka mradi kwenye kata, basi ni nzuri kata nzima kumaliza vijiji vyake vyote ili kisibaki kijiji na ikaonekana kama wametengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mfano, kwenye Kata ya Kiloleli yenye vijiji vinne, Kijiji kimoja kimeachwa, Kijiji cha Ilumya, lakini kwenye Kata ya Mwamanyili, Kijiji kimoja cha Milambe ambako Mbunge anatoka kimeachwa. Kwenye Kata ya Mkura, Vijiji viwili kwa maana ya Mwang’ale na Chabutwa vimeachwa. Kwa hiyo, nafikiri kwamba tunapokuwa tunafanya designing ya mradi kwenye kata husika basi ni vizuri kata nzima iweze kuchukuliwa na vijiji vyote viweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimefurahishwa sana na namna ambavyo wameanza kuleta mkakati wa mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Viktoria kwenda Itilima ambao kwa awamu ya kwanza utaanza na Busega, utaenda Bariadi lakini pia utaenda Itilima. Mradi huu ni mradi mkubwa na ndiyo mradi pekee ambao uta-solve tatizo la maji kwa Wilaya ya Busega, Wilaya ya Bariadi na Wilaya ya Itilima.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwamba, moja ya mradi ambao unatakiwa macho ya Waziri yaende hapo ni huu mradi mkubwa sana, kwa sababu hii miradi mikubwa unapokuwa umemalizika ni mradi ambao utahudumia wananchi wengi. Pale kwangu Jimbo la Busega zaidi ya vijiji 42 vinaenda kupitiwa. Mradi huu kwa Mkoa wa Simiyu utapita kwenye vijiji 256.

Mheshimiwa Naibu Spika,naomba na nimeona Waziri tayari ameweka kwenye Mpango bilioni 19 kwa ajili ya kuanza kati ya bilioni 400. Nimwombe kwamba awekeze sehemu hii ili wananchi wengi, zaidi ya 200,000 wa Wilaya ya Busega waweze kupata maji kupitia mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyokwambia sasa Wilaya ya Busega wananchi wanaopata maji safi na salama ni asilimia 52 wengine bado hawapati maji safi na salama na kijiji cha mwisho ni kijiji chenye kilometa 42, leo tunazungumza kuleta maji Dodoma zaidi ya kilometa 800 tunaomba na sisi utukumbuke kwenye kilometa 42 nao waweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja asilimia mia moja. Mheshimiwa Aweso karibu Usukumani, karibu Busega. Ahsante. (Makofi)
Hoja ya Dharura (Changamoto ya Kupanda kwa bei za Mafuta ya Petroli, Dizeli na Mafuta ya Taa)
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nijadili hili suala la dharura. Nimpongeze sana mtoa hoja kwa kutoa hoja hii ninaamini sasa sisi kama Bunge tunaenda kuishauri vizuri Serikali ili iweze kuchukua hatua. (Makofi)

Kama alivyosema Mheshimiwa Musukuma, kwamba sasa hivi mafuta yamepanda. Ukiangalia kwenye baadhi ya majimbo huko vijijini; kwa mfano kule ambako hakuna sheli (vituo vya mafuta sasa hivi kule mafuta yanauzwa zaidi ya shilingi 5,000. Jambo hili ni hatari kwa kuwa tunajua mafuta yanapopanda bei kila kitu kitapanda bei. Tunavyozungumza leo, jana kusafirisha cement kutoka Tanga kwenda Mwanza, hapo nyuma walikuwa wanasafirisha kwa tani moja shilingi 130,000 lakini tunavyozungumza leo tani moja ya cement kusafirisha kutoka Tanga kwenda Mwanza imepanda mpaka shilingi 160,000 ambapo inaenda kupandisha mfuko wa cement kwa shilingi 1,500 jambo hili ni kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishauri sasa Serikali kwa mambo mawili; jambo la kwanza ni kufanya hatua za dharura, kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka ruzuku kwenye mafuta ili walau tuweze kupunguza gharama za mafuta. Tukiweka ruzuku pale maana yake gharama ya mafuta inapungua, na ikishapungua hizi gharama za mafuta zitapunguza gharama za vitu vingine ambavyo sasa vitapanda bei.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, ninajua wazi kwamba tuna tozo nyingi ambazo tumeweka kwenye mafuta kwa ajili ya nchi na kwa ajili ya bajeti tuliyoipitisha. Lakini sisi ndio Wabunge na sisi ndio tuliyopitisha bajeti, hivyo kuna haja sasa ya kuangalia baadhi ya tozo tuweze kuziondoa kwa wakati wa dharura kwa hii miezi miwili; kwa maana ya mwezi wa tano na mwezi wa sita, tuzipunguze takribani kuanzia shilingi 400 mpaka shilingi 500 ili tuwe na unafuu kwenye mafuta. Tukiyafanya haya yataleta unafuu wa maisha kwa wananchi wetu, hamna namna ambayo tunaweza kufanya kwa sababu maisha ya kwetu tunayajua huko vijijini yanategemea mafuta; bila mafuta maisha hayaendi. Kwa sababu gani, kwa sababu leo cement itapanda, nondo zitapanda, sabuni zitapanda kila kitu kitapanda kwa hiyo, lazima tuchukue hatua za tahadhari za haraka ili kunusuru hili janga kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaomba sasa nami kuunga mkono hoja na tuweze kutafuta fedha za dharura tuweze kunusuru suala hili la dharura katika nchi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuchangia hotuba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami ninampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyokuja na mpango wa kuhakikisha kwamba tunawekeza sana katika Wizara hii, pia niwapongeze Waziri pamoja na Naibu kwa kazi kubwa ambayo mmeonesha kuanza kuifanya, pia nimpongeze sana Katibu Mkuu Shemdoe kwa kazi ambayo anaendelea kuifanya, akili kubwa aliyoitumia TAMISEMI basi akaendelee kutumia akili kubwa hivyohivyo kwenye Wizara ya Mifugo ili tuweze kupata pato kubwa kutokana na mifugo tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema mchango wa mifugo pamoja na uvuvi kwenye Serikali yetu ni asilimia saba ya pato la ndani, asilimia hizi ni chache sana ukilinganisha na idadi ya mifugo tuliyonayo. Ukichukua tu mifugo tuliyonayo inatosha kabisa kutupa pato kubwa ikilinganishwa na pato ambalo tunalipata sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifugo pia imekuwa ikiongezeka mwaka kila mwaka lakini pato ambalo linachangiwa kutoka kwenye Wizara hii linateremka kila mwaka. Kwa mfano, ukichukua 2016/2017 mchango wa pato ulikuwa asilimia 7.6, ukienda mwaka 2017/2018 asilimia 5.4, ukienda mwaka 2018/2019 asilimia 7.2, ukienda mwaka 2019/2020 asilimia 7.4, 2020/2021 asilimia Saba na 2021/2022 asilimia Saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haitoshi kuchangia asilimia Saba peke yake kutokana na mifugo pamoja na uvuvi, tunatamani kuona mwakani mchango wa Wizara hii unafika angalau asilimia 10, asilimia 12 mpaka asilimia 15 tuwekeze kwenye mifugo ni sehemu mojawapo pia ambayo tunaweza kupata rasilimali nyingi za fedha kutokana na Wizara hii ya Mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba sana Waziri angalia hili ni jambo ambalo tunatakiwa sasa tuwekeze kama ambavyo tumewekeza kwenye kilimo pia tuwekeze kwenye mifugo ili tuweze kupata pato kubwa litokanalo na mifugo. Kama walivyosema wenzangu pia hakuna tutakapokwepa kuwatambua wanyama, haiwezekani tukaacha kuwatambua wanyama halafu tunategemea kuongeza pato katika nchi yetu haitawezekana! Ili tuongeze pato katika nchi yetu ni lazima tuwatambue Wanyama, ni lazima tuwasajili Wanyama, pia ni lazima tuwafuatilie kwa sababu hatutaishia kwenye kuwatambua, unawatambua so what? Hatutaishia kwenye kuwasajili, unawasajili ili iweje? Tunatakiwa twende mbele zaidi kuwafuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta Afisa Mifugo yupo ofisini anaamka asubuhi hajui wala ratiba yake, hajui aende wapi, hajui aende kwa nani, hafahamu! Inatakiwa ifike sasa sehemu Afisa Mifugo akiamka asubuhi anajua kabisa kwamba naenda kwa mfugaji Songe ana ng’ombe 200, naenda kufanya kazi moja, mbili, tatu nne, tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tuwape elimu kwa sababu kama watakuwa wanafuga bila elimu, tutafuga ng’ombe 10,000 lakini mwisho wa siku tutaenda kwenye ‘inversely proportional to x’ tulikuwa tunasoma kwenye hesabu miaka fulani hivi kwamba x is inversely proportional to y, yaani kadri speed ya gari inavyoongezeka na muda unapungua. Kwa hiyo, kadri ya ng’ombe wanavyoongezeka wengi na pato nalo linapingua so what? Tunategemea ng’ombe wakiongezeka na pato liongezeke. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kuna muda mwingine lazima tuwasaidie hawa wafugaji, Mheshimiwa Waziri tuangalie sana kuwasaidia wafugaji, Maafisa Mifugo walioko huko wawe na ratiba ya kuwatembelea wafugaji ili wawasaidie, hata hili suala la hereni limefeli kwa sababu mwananchi anasema, so ukinivalishia hereni inakuwaje sasa? Wakipata Elimu mimi nafikiri ni jambo jema lakini kwa sababu hawajapate Elimu hawajui kwamba ukimvalisha heleni ng’ombe wake halafu mwisho wa siku inakuwaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza anatakiwa aambiwe tunataka tuwafahamu lakini pia tunataka tujue eneo hili kuna mifugo mingapi ili tuweze hata kuweza kutengeneza mabwawa kwa ajili ya maji, anajua oooh! Kumbe kutakuwa na faida, anajua kabisa kwamba hata yakitokea magonjwa anakuwa anafahamu kwamba eneo hili kuna ng’ombe kadhaa tupeleke dawa kadhaa, Hiyo ndiyo maana ya kuwatambua ng’ombe wetu ndiyo maana ya kutambua mifugo tuliyonayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri tuangalie, tuje na mpango ili tuweze kuwatambua. Niwaambie Watanzania wenzangu kama tunataka Pato la Taifa liongezeke kutokana na mifugo ni lazima tukubali kuwatambua mifugo, lazima tukubali kuwasajili mifugo, lazima tukubali kuwafuatilia mifugo bila hapo hatutapandisha pato kutokana na mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nichangie kidogo kwenye eneo la uvuvi. Mimi kila siku najiuliza kuna hawa watumishi ambao mmepeleka kwenye Wilaya zetu wanaotoka Wizara ya Uvuvi wako chini ya Katibu Mkuu Wizara ya Uvuvi ni sawa kabisa, lakini wakienda huko wanakuwa tofauti kabisa na Maafisa Uvuvi walioko kwenye Halmashauri, kila mtu utekelezaji wake anatekeleza tofauti. Huyu akienda huku anakuwa boss huyu akija huku anakuwa boss haiwezekani tukafika kwa stahili hiyo? Mheshimiwa Waziri liangalieni hili kama inawezekana wekeni agency, hawa waliopo Halmashauri waungane na hawa ambao wanatoka Wizarani wafanye kazi moja. Wanakamata watu, ukimuuliza ambae mimi namuuliza kila siku wa Halmashauri anasema sijui, kwa nini asijue wakati wanatekeleza wote sheria moja? Ni lazima wafanye kazi kwa Pamoja, ni lazima wafanye kazi kwa kushirikiana ili tusonge mbele na kuacha kuwanyanyasa wavuvi na kuwakatisha tamaa, tukitaka wavuvi wafanye kazi ni lazima tukubali kuwasaidia. Tukitaka wavuvi waweze kuleta pato katika nchi yetu ni lazima tukubali kuwapa semina, wamefika huko wanafika kukamata hatuwasaidii, nami nitakuwa wa mwisho kujisifu kuongeza pato eti kwa sababu ya faini, nitakuwa wa kwanza kushabikia kupunguza pato kwa sababu watu wametii sheria bila shuruti, hakuna sababu ya kujisifu kwamba tumekusanya hela nyingi zinazotokana na penalty tumekusanya fedha nyingi zinazotokana na faini maana yake makosa yameongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tusiwasaidie wavuvi kuwaelimisha badala ya kuwa na makosa mengi wawe na makosa kidogo ili tuweze kuwasaidia, tunawafilisi bila sababu za msingi. Halafu unakuta ana uvuvi haramu na huyu anaenunua nyavu dukani, hazijawahi hata kusikia mwenye duka kafilisiwa, hatujawahi kusikia mwenye kiwanda kafilisiwa lakini anaefilisiwa ni mvuvi kwani hamjui maduka yanayouza nyavu hizi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mnayajua maduka haya nendeni mkashughulike nao tuwasaidie wavuvi, tuwasaidie watu wa Busega, tuwasidie watu wa Mafia, tuwasaidie watu wa Mwanza ili waweze kuvua wakiwa na amani kuliko sasa hivi kila siku wamekuwa watu wa kukimbia kimbia, nakumbushwa hapa na Kigoma. Mheshimiwa Waziri tulifanye hili ili tuweze kuwasaidia, hamna sababu ya msingi ya kukimbizana na wavuvi, wanakufa humo ndani ya maji kwa sababu ya kukimbizana, tuwasaidie kuwashauri, tuwasaidie kuwapa semina, tuwasaidie kuwapa elimu, ikifika sehemu ya kumpiga faini basi tumpige faini lakini tuanze kwanza kwa kumsaidia huyu mvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni hilo la mikopo kwa vikundi vya wavuvi. Eneo hili na lenyewe lina ukiritimba mwingi bila sababu za msingi. Hebu Mheshimiwa Waziri angalieni hili, watu wa Busega huko wameomba mpaka wamechoka. Sasa wanaopewa hii mikopo ya vikundi ni watu gani tofauti na Watanzania? Tunaomba kama inawezekana, tu – review namna ya upatikanaji wa mikopo kwa ajili ya wavuvi wetu ili waweze kupata, kwani wameunda vikundi lakini upatikanaji unakuwa mdogo. Upatikanaji wake unakuwa wa kufuatilia, mwisho unafuatilia mpaka nusu ya gharama ya ule mkopo utakaopewa inaisha. Unafuatilia, unafuatilia, bila sababu za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri aangalie hili ili tuweze kuwasaidia wananchi hawa, ambao ni wavuvi ili waweze kuleta tija. Tunatamani mwakani akija hapa aseme mapato yamepanda kutoka asilimia saba ya mchango wa Wizara yake, imefika asilimia 10. Mimi nitakuwa wa kwanza kupiga makofi na wa kwanza kwenda kumpongeza nyumbani kwake, kwa sababu tutakuwa tumeona kweli amedhamiria kwa ajili ya Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie Bajeti ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2023/2024. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa namna ya pekee sana alivyoendelea kushusha fedha kwenye majimbo yetu, lakini pia kuendeleza miradi mingi ya kimkakati ambayo imekuwa na bajeti kubwa lakini tumeona haijaweza kusimama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana pia Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anazofanya katika Wizara ya Fedha pamoja na Naibu Waziri kwa kazi wanazofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo machache ambayo nataka kuchangia leo; jambo la kwanza nataka kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kuondoa ada kwenye Vyuo vya Elimu ya Kati. Hili jambo limepigiwa kelele muda mrefu sana, lakini leo sasa kwa bajeti hii wamekuja na muafaka wa wananchi wengi ambao walikuwa wakipiga kelele eneo hili. Tuwapongeze kwa sababu wamekuja na source ya kutafuta fedha kwa namna ya pekee ambavyo sasa wanaenda kuyakabili haya ambayo wameyaleta kwenye bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona eneo ambalo wamekuja nalo katika mwaka huu wa fedha unaofuata kwa ajili ya bajeti ya mwaka unaofuata, wamekuja na kuongeza shilingi mia kwenye mafuta. Jambo hili ni jambo zuri na tuna imani kabisa kwamba sasa tunaenda kuona matokeo na shilingi mia itakavyoongezwa kwenye mafuta. Kwa mfano, Busega tuna barabara inayotoka pale Nyashimo kuelekea Dutwa kwa Mheshimiwa Kundo kule. Tunaomba hii barabara itengenezwe kupitia fedha hizi ambazo tumeziweka ili wananchi wa Jimbo la Busega waone matokeo ya shilingi mia kwenye mafuta na barabara hii ni barabara muhimu sana kwenye uchumi wa wilaya hizi mbili kwa maana ya Wilaya ya Bariadi pamoja na Wilaya ya Busega. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuzungumza, sijui kama wameishafanya research ya kutosha kwa nini watu wanakwepa kutoa risiti na kwa nini watu hawadai risiti? Jambo hili ni jambo la kutiliwa maanani sana. Tuendelee kutoa elimu kwa walipa kodi, tuendelee kutoa elimu kwa wafanyabiashara ili waendelea kutoa risiti na hawa wananchi ambao wananunua vifaa na wenyewe waendelee kuomba risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nimekuwa nikifikiria, sijui kama mmeishafanya cost benefit analysis kwamba kiasi kinachopotea kwa kutokutoa risiti kwa maana ya mwananchi kutokudai risiti kile kiasi kinachopotea ukilinganisha na kiasi ambacho tunaweza kumpa mtu anapodai risiti kama token kwa yeye kudai risiti. Nilikuwa najaribu kufikiria, wanaweza kuunganisha mfumo wa risiti za EFD wakaunganisha na namba za simu za wananchi kwa sababu kila mwananchi ana namba ya simu, anapoenda kununua anataja namba yake ya simu, halafu kunakuwa na mfumo TRA na mwananchi anapokuwa amenunua na kupata risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ile risiti anapokuwa ameipata kwa mwezi mzima wanajua kabisa kwamba namba hii ya simu imepewa risiti kadhaa zenye thamani kadhaa wanam-credit bonus kwenye simu yake. Kwa sababu ameomba risiti hili jambo linaweza likawa zuri, hili jambo linaweza likawa na tija kwa mwananchi kuomba risiti. Kwa sababu mwananchi akiomba risiti ndipo atakuwa amechangia mapato katika nchi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaambie wananchi wa Tanzania kutokuomba risiti siyo kwamba wewe ndiyo unayenufaika, ananufaika yule muuzaji, kwa sababu ile kodi umemwachia, ile kodi anakula yule muuzaji kwa sababu hataipeleka TRA, kwa sababu hakuikatia risiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaweza kufanya hata mambo mengine kwamba, ile pesa wanaweza waka-credit kwenye kadi yake ya bima, wanaweza waka-credit kwa mwananchi ambaye hana, hapati mshahara kwamba anakatwa bima kupitia mshahara wake wakam-credit kwenye simu yake ikatumika kulipa matibabu yake. Hii itamwongeza mwananchi kujua kwamba ana haki ya kuomba risiti lakini mwananchi huyu huyu atajua kwamba nikiomba risiti mwisho wa mwezi nitapata credit ya manunuzi ambayo nimefanya. (Makofi)

Mhesjhimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mtu amefanya manunuzi ya shilingi milioni tatu, mwisho wa mwezi akapata credit ya shilingi elfu hamsini, anajua kabisa kwamba ninapoomba risiti mwisho wa mwezi nitapata credit kwenye simu yangu ya shilingi elfu hamsini. Naamini mapato ambayo tunayapoteza kwa wananchi kutokudai risiti ni makubwa kuliko mapato ambayo tutatumia kumpa mwananchi kama bonus kwa yule atakayekuwa ameomba risiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sasa Wizara ikae itafakari ione kama inafaa, basi tuwe na mfumo wa makampuni ya simu, mfumo TRA na mfumo wa hizi risiti tunazotoa ili ziweze kuwa na credit kwa mtu anapokuwa amenunua apate credit mwisho wa mwezi ili aone thamani ya kuomba risiti. Kwa sababu sasa hivi muda mwingine hawaoni thamani ya kuomba risiti ameenda kwa mfanyabiashara anaambiwa hii bidhaa nitakuuzia laki tisa, lakini bila risiti nitakuuzia shilingi laki nane na sabini ana-opt kutokuchukua risiti, lakini akijua kwamba nimefanya manunuzi ya kiasi fulani na mwisho mwezi nipata credit kutoa kwenye Serikali yangu, naamini kila mwananchi sasa atakuwa na morali ya kuomba risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasoma Ripoti ya CAG majuzi nikaona hata Serikalini. Serikali Kuu hawakuomba risiti yenye thamani ya bilioni 15, Mashirika ya Umma hawakuomba risiti za EFD milioni mia tano hamsini na siti, Serikali za Mitaa bilioni 10.08, jumla bilioni 25 hawakuomba risiti na ni watumishi wa Serikali. Hawa hawatufai, ni wahujumu uchumi kama wahujumu uchumi wengine, ni lazima sasa tuanze na Serikalini na wao wawe sehemu mojawapo ya kuhakikisha kwamba wanaomba risiti za EFD ili Serikali yetu ipate kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameeleza sasa ameongeza wigo wa usajili wa VAT kutoka turn over ya milioni mia moja kwa mwaka hadi turn over ya milioni mia mbili. Hili ni jambo zuri. lakini sidhani kama wamefanya utafiti mzuri wakaona kwamba turnover kuwa ndogo litaleta tatizo kubwa sidhani, tatizo kubwa ni wafanyabiashara kukwepa kodi. Kwa sababu duka A yeye hajasajiliwa VAT, duka B amesajiliwa VAT, mauzo huyu item ile ile anauza shilingi elfu mbili na kwa sababu hajasajiliwa ile VAT anauza elfu mbili, aliyesajiliwa na VAT inabidi aongeze asilimia kumi na nane, atauza elfu mbili mia tatu sitini, lazima huyu atauza zaidi kuliko huyu, nini kinatakiwa kufanyika hapo? Hapa jambo siyo kuongeza tu…

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Sekiboko, taarifa.

TAARIFA

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Simon ameweka mchango mzuri sana, lakini nimpe taarifa kidogo kwamba kuongeza wigo wa VAT kunam-comfort mfanyabiashara kutoa risiti ya EFD bila kuogopa kufikia ukomo wa milioni mia kwa mwaka. Jambo ambalo litaongeza mapato zaidi kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Simon, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea, lakini sidhani kama ni tija sana, ninachotafuta hapa, natafuta fairness ya wafanyabiashara. Kwa sababu turn over ya milioni 180 haina tofauti kubwa na turn over ya milioni 210. Huyu mwenye turn over ya milioni 210 anakuwa amesajiliwa na huyu mwenye turn over ya milioni 190 yeye hajasajiliwa, lakini unakuta wanauza item ile ile. Huyu anauza simu hii hii na huyu anauza simu hii hii, huyu lazima auze bei ndogo na huyu lazima auze bei kubwa sababu ana VAT.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa kinachotafutwa ni kuwasababisha hawa wafanyabiashara kila mtu ajue kwamba kuna fair kwenye kodi. Nataka kumshauri Mheshimiwa Waziri, hapa ili kila mtu awe na fairness katika kulipa kodi wasajiliwe watu na VAT haijalishi turn over ni milioni 50 ili kila mtu sasa ajue kabisa kwamba hapa bei ya simu ni shilingi 200,000 na hapa bei ya simu ni shilingi 200,000, hakuna sababu ya kukwepa kutoa risiti kwa sababu wote mnauza bei sawa. Huyu anakwepa kutoa risiti kwa sababu anajua akitoa risiti itabidi aongeze asilimia 18 na mteja atamkimbia, ataenda kwa mtu ambaye hajasajiliwa na VAT kwa sababu anajua yeye hatachajiwa ile asilimia 18. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ili kuwe na fairness naishauri Wizara itafakari na ifanye upembuzi yakinifu ikiona inafaa wasajiliwe watu wengi regardless of the turnover ili watu wengi waone kabisa kwamba there is fair katika biashara na waache kukwepa kodi. Ninachozungumzia hapa ni kuacha kukwepa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona umewasha microphone. Naomba niunge mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kunipa nafasi hii nami nichangie Wizara hii ya Mifugo na Uvuvi, lakini kipekee nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wanafanya pamoja na Watendaji Wakuu wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, leo nataka kuchangia tu mambo mawili katika Wizara hii ya Uvuvi. Hapa nyuma kidogo tumekuwa na wimbi kubwa la upungufu au uhaba wa samaki viwandani, leo nataka niishauri Wizara jambo mojawapo ambalo linalosababisha kuwa na uhaba wa samaki katika viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, ijulikane ya kwamba tuna samaki aina ya sangara hasa kwenye Ziwa letu la Victoria na samaki huyu kwa kilo moja anauzwa shilingi 9,000 mpaka shilingi 10,000 pale Mwaloni. Sasa chukulia samaki wa kilo tano kwa shilingi 9,000 atauzwa shilingi 45,000; lakini ijulikane ya kwamba bondo ndani ya ile samaki ndio lenye samani kubwa kuliko mnofu. Sasa wanapokuwa wanauza pamoja na bondo lake kwa shilingi 9,000 na akipeleka kiwandani atauza kilo moja kwa shilingi 12,000 ina maana kwa samaki mwenye kilo tano atamuuza shilingi 60,000; lakini bondo linauzwa zaidi ya shilingi 60,000 samaki mwenye kilo tano.

Mheshimiwa Spika, sasa mvuvi amekuja na option ambayo ni ya kawaida tu kwamba badala ya kumpeleka yule samaki kiwandani bora mnofu wake awauzie wananchi halafu yeye anufaike na lile bondo. Anajikuta kwa wananchi anaweza kumuuza yule samaki wa kilo tano mpaka shilingi 40,000 mpaka shilingi 50,000 na bondo pia akauza kwa shilingi 50,000.

Mheshimiwa Spika, hapo atajikuta ameingiza shilingi laki moja kwa samaki mwenye kilo tano, lakini atakapompeleka kiwandani atamuuza kwa bondo lake kwa shilingi 60,000 hata ningekuwa mimi nisingeweza kupeleka samaki yule kiwanda.

Sasa mimi niishauri Wizara, waruhusiwe wavuvi au wafanyabishara ambao wanapeleka samaki kiwandani basi kuwepo na thamani ya mnofu na thamani ya bondo liuzwe peke yake, hii itasababisha kunufaisha huyu mvuvi kwa sababu thamani ya samaki itaongezeka, na kama hazitafanya hivi maana yake wataendelea hao wavuvi kutaka samaki vipande vidogo vidogo, wanawauzia wananchi na viwanda nyetu vitaendele kuwa na uhaba kama ambavyo imeonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia ijulikane ya kwamba matumizi ya ndani yameongezeka ya watumia samaki kama kitoweo hata marafiki zangu hapa Wagogo wanataka samaki kutoka Ziwa Victoria kule Usukumani, sasa ni lazima tu viwanda vikose samaki. Kwa hiyo mimi niishauri Wizara kwamba pia lazima tujikite sana kwenye mabwawa ili tuendelee kupata samaki wengi na hawa samaki waweze kutumika katika matumizi yale ya kawaida ya ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia kupunguza ukiritimba hawa wawekezaji wanapokuja kwa ajili ya vizimba, ukija na kizimba utapewa masharti makubwa, tafute eneo kijijini, nenda katafute kibali, lete mtu wa TAFIRI aje apime, huu mlolongo unasababisha wawekezaji wanaondoka; nilitamani sana Wizara iliangalie hili ili mwisho wa siku tuwe na malighafi ya kutosha kwenye viwanda vyetu.

Mheshimiwa Spika, lakini suala lingine ambalo nilitaka kushauri ni tozo kwa wavuvi; kuna tozo nyingi hapa kwa wavuvi kuna tozo inayotozwa na TASAC ambao wanakuja kukagua ubora wa mtumbwi wanatoza shilingi 70,000.

Mheshimiwa Waziri umefika pale kwangu ulikuja wananchi walikulalamikia na ulisema utalishulikia hili lakini bado halijashughulikiwa bado wanatoza shilingi 70,000 kukagua ubora wa mtumbwi. Sasa hapa wananchi wangu wameniuliza swali ndogo sana kama leo mtumbwi ni mpya unakuja kukaguliwa nalipa shilingi 70,000 wakati ni mpya wala haujatumika, sasa wanakagua ubora upi wakati bado ni mpya.

Mheshimiwa Spika, hili swali ni very technque kidogo, mimi niishauri Wizara kwamba wananchi wetu hawajakataa kulipa, lakini wanaona shilingi 70,000 ni kiwango kikubwa sana ukilinganisha na kazi ambayo inakuja kufanyika. Kwa hiyo niiombe Wizara iweze kuliangalia hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna tozo kama leseni ya mtumbwi inayotozwa na halmashauri shilingi 30,000 lakini pia kuna leseni kwa mvuvi mmojammoja shilingi 20,000 hapa pia na penyewe nilitamani sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika naunga mkono hoja, lakini tuangalie bei ya samaki ukilinganisha na bondo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nami nikupongeze kwa kuwa Mwenyekiti. Nakutakia mema sana katika kazi hiyo. Pia nichukue fursa hii adimu sana kumpongeza Waziri, mtani wangu kwa kazi kubwa sana anayoifanya kwa jamii yetu hii ya Tanzania. Kipekee nampongeza Naibu Waziri kwa kazi
kubwa pia anayofanya na kweli ameonesha hekima kubwa sana hata leo asubuhi, ameonesha upendo wa dhati sana kwenye Wizara yake na hiyo ndiyo tumeona faida kubwa sana ya kuzaliwa usukumani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie mambo machache sana kwenye Wizara hii leo. Naishauri sasa Wizara, leo asubuhi hapa Mheshimiwa Mrisho Gambo amesema asilimia 80 ya mapato ya Wizara ya Utalii yanapatikana kule Kanda ya Kaskazini. Hata hivyo, tunaamini kabisa kwamba Kanda ya Ziwa pia tunaweza kuwa na mapato makubwa ya utalii mkitufanyia mambo ya msingi sana ikiwemo na kufungua geti la Ndabaka lililoko pale Lamadi na pia mtufungulie geti la pale Kijereshi. Mageti haya mawili yatakuwa mageti ya msingi sana kwenye pato la Taifa; vile vile yatakuza uchumi wa Kanda yetu ya Ziwa, yatakuza uchumi wa pale Jimbo langu la Busega, hasa pale Lamadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna hoteli nzuri sana Speke Bay, tuna hoteli nzuri pale Serenity na pia tuna hoteli nzuri pale Ndabaka, zina uwezo kabisa wa kutunza watalii. Naomba mtufungulie yale mageti ili yaweze kupokea watalii mbalimbali. Watalii siyo lazima waende KIA, wanaweza kushukia pale Mwanza Airport na baadaye wakaenda Lamadi kwa ajili ya kufanya tour pale Serengeti.

Kwa hiyo, nawaomba sana, mkitufungulia haya mageti mawili yatafanya kazi kubwa sana ya kukaribisha wale watalii na hasa mkiyatangaza. Myatangaze ili watalii wetu sasa waweze kupitia pale kwenye geti la Ndabaga lililopo pale Lamadi na geti la Kijereshi lililoko kule Kata ya Mkura.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nichangie ni uvamizi wa tembo kwenye makazi ya watu. Pale kwangu kuna Kijiji kinaitwa Kijereshi, kuna Kijiji kinaitwa Lukungu, kuna Kijiji kinaitwa Mwakiroba vijiji hivi vitatu vinaathirika sehemu kubwa sana na uvamizi wa tembo. Naomba sasa mchukulie hatua za dharula ili wananchi wetu sasa waweze kutokutishwa na hawa tembo. Mwaka 2020 tulikuwa na vifo zaidi ya vinne vilivyotokana na uvamizi wa Tembo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, leo nakuomba sana Mheshimiwa Waziri, wewe ni msikivu, naomba sana kwa mara nyingine tuweze kuangalia namna ya kuleta askari wa kutosha tuweze kutengeneza Stesheni pale Kijereshi ili maaskari waweze kukaa pale. Ikibidi linapotokea tatizo, basi wapatikane kwa urahisi kwa sababu sasa hivi wanakaa Lamadi na Kijereshi ni mbali kidogo, tembo wanapoingia kule Kijereshi, wao mpaka waje wafike ni zaidi ya nusu saa muda mwingine, mpaka saa nzima au saa 1.30 ndiyo wanafika. Tembo tayari watakuwa wameharibu mazao, tayari watakuwa wamewadhuru wananchi.

Kwa hiyo, naomba sana, mtengeneze Stesheni pale Kijereshi kwa sababu ndiyo sehemu kubwa ya hifadhi. Pia muwape gari pale. Kuna shida ya gari kwa ajili ya usafiri wa kukabili hawa tembo. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri atusaidie hili ili tuweze kupata gari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nililotaka kuzungumzia ni tatizo la TFS. Mheshimiwa Waziri, TFS ni pasua kichwa kwa baadhi ya watumishi; kuna baadhi ya watumishi sio waadilifu. Ukienda pale Magu, kuna TFS ambao wanalinda Hifadhi ya pori la Sayaka. Pale ni pasua kichwa. Wanakamata wafugaji, ni sawa inawezekana wanasimamia sheria, lakini faini ni kubwa sana. Ni shilingi milioni sita, shilingi milioni nne au shilingi milioni nane. Ni tatizo kubwa. Naomba sana tuliangalie hili, mfugaji akiambiwa kulipa shilingi milioni sita leo, haiwezekani. Mfugaji akiambiwa kulipa shilingi milioni nne leo haiwezekani; yaani how much is milioni nne? Yaani ni fedha nyingi kweli kwa mfugaji mdogo. (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba hawa watumishi kidogo wanapokuwa wanalingalia hili, wawahurumie na wafugaji wetu, wawahurumie na wakulima wetu kwa sababu wanaumizwa sana na faini ambazo wanapigwa. Mheshimiwa Waziri, nimeshazungumza, nawe umeshakubali kuja pale, uje ujionee namna wananchi walivyo na malalamiko juu ya hifadhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nakuomba sana, wananchi wale walikuwa na shida ya eneo la mita 840. Naomba sana utakapofika pale uzungumze na wananchi, usikie kilio chao na kama utaona inafaa Mheshimiwa Waziri, basi muweze kuwarejeshea eneo hili ili watu wa Nyaruande pale Kata ya Nyaruande katika Jimbo langu la Busega na sehemu ya Jimbo la Magu waweze kunufaika pale Sayaka kwa sababu sasa hivi wanapata shida katika namna ya kupata sehemu za kuchungia ng’ombe, lakini pia sehemu kubwa ya kulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri; wewe kule ni kwenu, wewe pale ndiyo umezaliwa, hili tatizo unalifahamu, njooni mlitatue ili wananchi wetu sasa waweze kunufaika na hii sehemu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nskushukuru sana, niseme nawapongeza, nawakaribisha Busega mje mtatue huu mgogoro. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hotuba ya Waziri wa Mifugo na Uvuvi lakini kabla yayote nikutakie heri sana katika siku yako ya leo ya kumbukizi ya siku ya kuzaliwa.

NAIBU SPIKA: Ahsante bwana. (Makofi)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anazofanya kwa ajili ya nchi yetu pia nimpongeze kaka yangu Mashimba na Mtani wangu Mheshimiwa Ulega kwa kazi ambazo wanafanya katika Wizara hii ya Mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilipokuwa nasoma bajeti hii ya leo na bajeti iliyopita nimejifunza suala moja. Kila siku Waziri wa Maji Mheshimiwa Aweso hapa amekuwa akisema wali wa kushiba unauona kwenye sahani lakini leo ninaona wali wa kushiba sijauona kwenye sahani kwasababu bajeti ya Maendeleo Sekta ya Uvuvi 2021/2022 tulipanga Bilioni 99 mpaka Aprili, 2022 fedha zilizopelekwa kwenye Wizara ni bilioni 3.9 sawa na asilimia Sita, hii haiwezekani!

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamuomba sasa Kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Waziri wa Fedha aangalie Wizara hii kwa macho mawili kwa sababu kuna baadhi ya Wilaya kama Busega, chanzo cha mapato ni uvuvi. Kama wananchi wetu hawatapelekewa fedha kwa ajili ya uvuvi maana yake hatujataka kuwasaidia. Kwa hiyo, tukitaka kuwasaidia Watanzania wavuvi lazima tupeleke fedha kwenye Wizara ya Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilivyokuwa najaribu kufikiri namna ya kuchangia kwa Kaka Mashimba nikasema nitamuonea bure, bali nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha aangalie namna ya kuwasaidia watu wa Wizara ya Mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lipo jambo moja ambalo naomba nilichangie kwa msisitizo. Kuna hawa watu wanaitwa BMU yaani Beach Management Unit, wamekuwa ni shida kwenye taasisi zetu, wamekuwa ni shida kuanzia kwenye Halmashauri lakini wamekuwa ni shida mpaka kwa Wavuvi, sasa wamebadilisha namna ya kufanyakazi zao wanaanza kuwasumbua wavuvi usiku na kuwabambikizia kesi na kesho asubuhi kuwapiga faini isiyopungua milioni tano hii kitu haiwezekani ni lazima tufikirie namna iliyobora kwa ajili ya kulinda rasilimali za nchi hasa samaki bila kutumia nguvu nyingi ambazo leo wanatumia hawa BMU. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ninaishauri Wizara ifanye mpango mkakati mzuri zaidi wa kuangalia namna ya kutunza na kuangalia hizi rasilimali za Ziwa kwa kutokuwatumia hawa watu ambao wanatusumbua sasa hivi, wavuvi wanawakimbia wanapigana na Mheshimiwa Ulega, nafikiri Bunge lililopita nilikuletea hizi kesi kuna watu Wanne walikufa kwa sababu ya kupigania na hawa watu wa BMU ni lazima tutafute namna iliyobora ya kuwasaidia Watanzania, namna iliyobora ya kuwashauri hawa wavuvi kutumia nguvu ambayo ni rafiki na isiwe nguvu ambayo ni hasi na kuendelea kupata maafa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hili jambo pia kuna Maafisa wa Uvuvi kutoka Wizarani, hawa watu wanapoenda kwenye Wilaya zetu wanakuwa watu tofauti kabisa na Maafisa Uvuvi wa Halmashauri, unafikiri ni taasisi mbili tofauti, utafikiri ni nchi mbili tofauti, hawa watu wa Wizara wanakuja na sheria zao, watu wa halmashauri kuna Afisa Uvuvi nae ana sheria zake, anafahamu hivi, hawa wanafahamu hivi wanawatesa wavuvi bila sababu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ninakuomba haya malalamiko tumeyaleta, tunaomba Maafisa wanaotoka kwenye Wizara ya Uvuvi, wanapofika kwenye Halmashauri zetu wawasiliane na Maafisa Uvuvi wa Halmashauri ili wawe kitu kimoja kwa ajili ya utekelezaji wa kazi ambao mtakuwa mmewatuma kwenda kufanya. Mimi kama Mbunge nikimuuliza Afisa wa Halmashauri anasema mimi sijui, siyo maagizo ya Wizara lakini Wizara wanasema haya ndiyo maagizo ambayo tumepewa sasa mnawatuma hivyo ni lazima waende wakashirikiane na watu wa Halmashauri ili wafanyekazi iliyobora na haya itatusababishia sasa wananchi wetu waweze kujifunza kupata elimu chanya kutoka kwa hawa watu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimekuwa nikiwaza mara nyingi tunapokuwa tunakomesha uvuvi haramu na tunaenda kumkatamata mvuvi, tunaenda kukamata samaki sasa najifikiria suala moja, hivi tumeshawahi kufikiria hao wanaoleta hizi nyavu? Tumeshawahi kufikiria juu ya viwanda, hivi inakuwaje mvuvi anaenda kununua nyavu na mwisho wa siku anaenda kukamatwa lakini kuna mtu ameingiza nyavu kapitia bandarini, kuna kiwanda kinatengeneza nyavu kipo Tanzania, haiwezekani katika akili ya kawaida! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lazima Wizara sasa ifanye jukumu lake, kama kuna kiwanda kinatengeneza nyavu ambazo si halali ni lazima tuanzie huko kwenye chanzo badala ya kwenda kumsumbua Mtanzania ambaye inawezekana ni layman kama mimi, hajui chochote hata hizo tunazoita sentimeta Sita za nyavu yeye hajui, anapewa nne lakini kumbe ninyi mnataka sita na mwisho wa siku mnamkamata na faini Milioni 20! Mtanzania anauza nyumba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana kwenye hili tuanzie kwenye viwanda, tuanzie kwa watu wanaoingiza hizi nyavu, najua Ulega upo smart kwenye kukesha, nenda kakeshe bandarini, nenda kakeshe huko kwenye viwanda kuhakikisha kwamba hawa wanaoingiza nyavu ambazo siyo salama muanze nao huko kabla hamjafika kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia najifikiria swali moja, samaki anaenda kukamatwa pale sokoni kapita tayari Ziwani kuna mtu kakatisha ushuru, kachukua hela ka-deposit hela za Serikali tayari lakini mwisho wa siku mtu anaenda kukamatwa kwamba samaki siyo saizi inayotakiwa! Sasa najiuliza huyu aliyechukua ushuru wake yeye hawakuwaona hawa Samaki? Ni Mtanzania huyohuyo tunampa hasara mara mbili, Lazima tutafakari kama samaki alikuwa na shida, shida ianzie ziwani palepale na asiende kukamatwa kule sokoni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine nichangie kwenye suala zima la mikopo. Siku zote tumekuwa tukiambiwa kuna mikopo ya wavuvi lakini wavuvi wa vijijini kama Busega hawanufaiki na hii mikopo, hawanufaiki na mikopo ya vikundi kwanini? Kwa sababu sijajua kama hii mikopo inaishia Mjini kule Vijijini haifiki. Mheshimiwa Waziri Mashimba nilishakufikia, nilishakuambia suala hili tusaidieni wananchi wetu nao waweze kunufaika na mikopo inayotolewa na Wizara yako ili waweze kupata vifaa vya uvuvi kama vile engine, kama vile nyavu waweze kununua kutokana na ile mikopo ambayo mtakuwa mmewapa. Niombe sana suala hili tulichukulie maanani lakini kama itabidi Wizara yako watu watoke maofisini waende huko site wakawafundishe namna ya kuunda vikundi ili hawa watu waweze kujua namna ya kuunda vikundi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani sana Wizara yako sasa iamke kuhakikisha kwamba tunaenda kufanyakazi yenye tija kwa wananchi hasa wa Jimbo la Busega ambako kuna Ziwa nawewe bahati nzuri umefika mahapa pale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ulifika pale Nyamikoma tukiwa na wewe, alianza kufika Mheshimiwa Mpina akiwa Waziri wa Mifugo na Uvuvi lakini pia na wewe ulivyoteuliwa tu ulifika pale Nyamikoma. Mliahidi kuwepo na mwalo wa kisasa, kwenye bajeti ya mwaka jana mliweka fedha kwa ajili ya ujenzi wa mwalo lakini mpaka sasa hivi tunavyozungumza hakuna kinachoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefika ofisini kwako nimepata majibu kwamba mmetangaza Mkandarasi, ninavyokwambia mpaka leo hakuna cha Mkandarasi, hakuna kinachoendelea katika mwalo wa Wanyamikoma. Ninakupongeza katika mwalo wa Ihale angalau kazi imefanyika pale tulipata milioni 162 ninakushukuru sana Ulega ulifika pale tukapiga siasa kidogo, wananchi wakafahamu juhudi ambazo unazo, lakini sasa tumalizie na huu mwalo ambao tumekuwa tukiuahidi zaidi ya awamu tatu. Mheshimiwa Mpina aliahidi pale nafikiri ilikuwa mwaka 2018 na wewe Mheshimiwa Mashimba umeahidi pale 2021 sasa tuende tukafanye kazi tupate fedha ili tuweze kutengeneza ule mwalo wa kisasa kama ambavyo uliahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna suala ambalo nilichangia hata bajeti iliyopita. Mmekuwa mkisema kuna ukosefu wa samaki viwandani. Nami nafikiria suala moja, tutaendelea kusema hakuna samaki kwenye viwanda vyetu kwa sababu ya bei ya samaki. Hakuna mwananchi ambaye anateseka usiku kucha ataenda kuuza samaki kilo moja kwa Shilingi 8,800/=. Hakuna mwananchi atakayeenda kuuza samaki kilo tano, kwa maana ya kilo moja kwa Shilingi 11,500 likiwepo na bondo lake, haitawezekana, kwa sababu bondo lina bei kubwa. Mwananchi anaamua sasa bora agawe zile samaki kipande kipande, auze kidogo kidogo, lakini mwisho wa siku anufaike na bondo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilishauri Wizara mwaka 2021, mkitaka kufanikisha eneo hili na kuwasaidia Watanzania, ni lazima ijulikane kiwandani, bei ya mnofu ijulikane, na bei ya bondo pia iweze kujulikana. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Simon.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa na Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha uliuoishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Seriakli za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishi tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezajiwa wa Mitaji ya Umma kuhusu uwekezaji wa mitaji ya umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie taarifa ya Kamati zetu zote tatu. Kitu ambacho nimejifunza kwa Serikali kwa wakati huu, kidogo sana, uandaaji wa hesabu ufanisi umeongezeka. Kwa kweli tunawapongeza Serikali kwa kuongeza ufanisi katika suala zima la uandaji wa hesabu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo, kuna changamoto ambazo zimeonekana na bahati nzuri Kamati zetu zimetoa hapa. Nitachangia maeneo matatu. Eneo la kwanza, ni eneo la Mfuko wa Pembejeo; limesemwa na Kamati ya PAC lakini pia limesemwa na Kamati ya PIC. Haiwezekani kwa akili ya kawaida. Haiwezekani kabisa mnakopesha shilingi bilioni 26, halafu katika zile shilingi bilioni 26, shilingi bilioni 21 zinakuwa na indication ya kutokukusanyika. Hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naona hapa ufanisi wakati wa utoaji wa mikopo hii haukuwa vizuri, kwa sababu kama tungefanya due diligence vizuri katika utoaji wa mikopo hii isingewezekana leo tunazungumza shilingi bilioni 21 ni mikopo chechefu yaani NPL, tunaweza kuzungumza mikopo mmetoa shilingi bilioni 26 katika zile shilingi bilioni 26, shilingi bilioni 21 hazikusanyiki hii haiwezekani! Nimeona Kamati ya PIC wametoa pendekezo la kufuta mikopo hii, mimi nitakuwa wa mwisho kukubaliana na hili, watu hawawezi kukopeshwa shilingi bilioni 21halafu leo tupitishe tufute eti tu-write off kwenye vitabu vya hesabu, fedha za Serikali ziwe zimekufa kiasi hicho, haiwezekani tufanye suala kama hilo. Watu waliokopeshwa wafuatiliwe, fedha zetu za Serikali zirudi tukopeshe watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano 2003 mpaka 2017 kuna bank zilikopeshwa zaidi ya shilingi milioni 800 zikafungwa na mikopo hii ikafia huko. Mfano, kulikuwa na Benki inaitwa Kagera Cooperative Bank, ilikopeshwa shilingi milioni 294, kulikuwa na Benki inaitwa Mbinga Community Bank ilikopeshwa shilingi milioni 286. Kulikuwa na Benki inaitwa Meru Community Bank ilikopeshwa shilingi milioni 150, kulikuwa na Benki inaitwa Njombe Community Bank ilikopeshwa shilingi bilioni 76. Hawa wote hawakurejesha fedha hizi! Pamoja na hayo nini kifanyike? Leo hatuwezi kupitisha eti tufute madeni haya Hapana! Maafisa Masuuli wahakikishe fedha hizi za walipa kodi, fedha hizi za nchi yetu ya Tanzania zinarejeshwa ili watu wengine waweze kukopeshwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, benchmark ya mikopo inasema “mikopo chechefu walau iwe asilimia tano” yaani mikopo ambayo inaweza isikusanyike walau iwe asilimia tano. Kwa Mfuko wa Pembejeo ni asilimia 81, sasa asilimia 81 na sisi tuunge mkono eti tu-write off kwenye vitabu vyao vya hesabu, haiwezekani! Tunaomba sasa Wizara pamoja na Mfuko wetu wa Pembejeo, wahakikishe fedha hizi zinarejeshwa. Pia wafanye due diligence wakati wanatoa mikopo kwa Watanzania, inawezekana wanatoa mikopo halafu wanaenda kuzichukua zile fedha, halafu waliopewa wanashindwa kurejesha na tunafika kwenye hali ambayo leo tumefika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lazima tuimarishe mfumo wa ndani wa ukusanyaji. Tulipowahoji hao watu walisema mfumo wa ndani wa ukusanyaji wa hizi fedha siyo mzuri, pia wanasema staff ni watu wachache. Sasa kama staff ni watu wachache inakuwaje tunakopesha? Kwa hiyo, tanakopesha halafu tunakuja kusakizia eti hatuna watu wa kufuatilia hiyo mikopo, kweli? Haiwezekani ni lazima tuhurumie fedha za walipa kodi, ni lazima tuhurumie fedha anazotupatia Mama yetu kipenzi Mama Samia Suluhu Hassan, analeta fedha nyingi lazima sisi tuwe mfano wa watu ambao tunakusanya fedha hizi ili kusudi ziweze kuzunguka kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni eneo la TANOIL, Shirika letu la Mafuta. Hapa sasa ndiyo kuna issue, kilichofanyika nini hapa? Tumepata hasara ya shilingi bilioni saba na milioni mia nane. Hasara hii imetokana na nini, hasara hii imetokana na watendaji kujichukulia uamuzi ambao haupo katika kanuni ambazo zinawaongoza. Kanuni zinataka uuze kwa bei hii, lakini wao wanajichukulia maamuzi yao binafsi kupunguza bei ya mafuta kwa lita ambayo haipo kwenye kanuni. Pale TANOIL wanakanuni kwamba, ile margin wanaweza kupunguza kwa asilimia 30, lakini imefika sehemu mpaka wanapunguza zaidi kwa shilingi 78 mpaka kupelekea kupata hasara ya shilingi bilioni 7.8.

Mheshimiwa Spika, tulipowauliza walipata wapi kibali, hawana kibali. Waziri wa Nishati, hakuwapa kibali, TPDC hakuwapa kibali. Wakajichukulia tu wenyewe, Bodi haikuruhusu lakini wao wakaamua tu kupunguza bei ya mafuta, haiwezekani, implication yake ni nini? Implication yake hii kwa wale ambao sasa wanawauzia mafuta, wanawauzia kwa kuwapunguzia kwa sababu wao wameamua halafu wanatuzunguka wanaenda kuchukua cha juu, business as usual. Lazima tuangalie hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bahati nzuri, Waziri wa Nishati yupo hapa, naomba akaanze na hili, ni lazima tukubaliane na pendekezo la Kamati, Mkaguzi Mkuu akafanye ukaguzi wa kiuchunguzi yaani Forensic Audit kuona wale wote waliosababisha hasara kwa Taifa ya shilingi bilioni 7.8 wachukuliwe hatua za kinidhamu, bila hivyo tutakuwa tunapeleka fedha, tunafanya biashara lakini hatupati faida, tunafanyeje sasa, tunakuwaje na kampuni ambayo leo imetuingiza hasara ya shilingi bilioni 7.8 halafu bado ipo. Haiwezekani lazima tuchukuwe maamuzi ya kuwasaidia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu na la mwisho. Kampuni ya Mbolea, yaani hawa watu wanafanya biashara ya mbolea katika mwaka ambao tunauzungumza 2021/2022, Serikali ilipeleka ruzuku kwa kampuni ya mbolea ya shilingi bilioni 10 kwa ajili ya kulipa mishahara pamoja na operating expenses. Katika biashara waliyofanya, hawakufanaya biashara yoyote wakapata sales sifuri. Yaani tumepeleka fedha watu wamekaa ofisini, wamelipwa mishahara shilingi bilioni 10.2, mishahara imelipwa kwa watu, matumizi ya mafuta tumewapa, sasa walikuwa wanafanya nini? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, yaani sales ni sifuri, wanafanya nini, si tuwapeleke wakafanye kazi zingine? Tuwapeleke hata huko Busega wakatusaidie kazi zingine? Kwa hiyo tuyaangalie maeneo haya. Hatuwezi tukawa tunapeleka fedha za Serikali, tunalipa watu mishahara halafu wanasoma magazeti, haiwezekani ni lazima mishahara ilete tija kwa Taifa. Sisi Wahasibu tunaita this is nugatory expenditure, you incur some expenditure that cannot generate any benefit! Ndiyo hawa wa mbolea, tumegharamika shilingi bilioni 10 hakuna walichotuingizia Serikalini. Yupo Mkurugenzi Mkuu, yupo sijui Afisa nini wanaitwa, yupo Afisa Masoko, Afisa sijui nani, sasa hawa wanafanya nini huko? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kampuni ambazo tunazianzisha ni lazima zilete tija, zilete matokeo kwa Watanzania. Kama kuna kampuni, kama kuna Mfuko hauleti matokeo chanya kwa Watanzania, kama hauleti matokeo chanya kwa Taifa ni heri ufutwe kuliko kuendelea kutuingizia hasara bila sababu za msingi. Mfuko wa Mbolea umetuingizia hasara bila sababu za msingi, futeni pelekeni Wizarani watagawa mbolea, kuliko kupeleka fedha shilingi bilioni 10.2 halafu mwisho wa siku hamna mapato ambayo tunapata kama nchi, hamna biashara wanayofanya, tumewapa mafuta, tumewalipa posho halafu kwenye hizi kuna posho nyingi, karibu shilingi milioni 800, tulipowauliza za nini sijui walikuwa wanafuatilia! Sasa unafuatilia nini wakati hakuna ulichouza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasikia kengele ya pili naomba kuunga mkono hoja mapendekezo yote ya Kamati yachukuliwe kama yalivyo, Forensic Audit kwa TANOIL lazima ifanyike. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nami kwa kunipa nafasi kuchangia Mpango wa Bajeti 2022/23.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee sana nimshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayofanya kwa ajili ya Watanzania. Kipekee pia nimshukuru kwa fedha ambazo ametupatia hivi karibuni kwenye majimbo yetu, trilioni 1.3 katika sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuchomekea hapo eneo la elimu. Ni kweli kuna kazi zinafanyika kubwa kwenye Majimbo sasa, madarasa yanajengwa, tunamshukuru sana. Lakini ukweli lazima tukubaliane kujengwa kwa madarasa lazima kuwe directly proportional na upatikanaji wa Walimu. Kwa hiyo mimi niishauri Serikali ije na mpango katika Bajeti ya mwaka 2022/23 wa namna gani tunakwenda kuajiri walimu ili wakabiliane na wanafunzi wengi ambao wanakwenda kutumia madarasa haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tunavyokuwa tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutupatia madarasa pia tunamshukuru kwa sababu ni imani yangu kwamba tunakwenda ku-create ajira kwa ajili ya Watanzania na Walimu ambao bado hawajapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichangie maeneo machache sana ya mpango huu. Taarifa ya Kamati ya Bajeti pamoja na taarifa ya Mheshimiwa Waziri imeonesha kwamba mwenendo wa Shilingi yetu ya Tanzania unazidi kuimarika. Lakini niseme tu kwamba ili shilingi yetu iendelee kuimarika zaidi ni lazima tufikirie ku-export final product kuliko kuwa na importation kubwa ya raw material kwa ajili ya viwanda vyetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa nini tunazungumza hivi? Ni lazima tuimarishe viwanda vyetu vya ndani na kuendelea kujenga viwanda mbalimbali ambavyo vitatoa final product kutokana na malighafi ambayo sisi wenyewe tunatengeneza hapa, malighafi nyingi zipo zinatokana na kilimo. Tuchukulie mfano kule kwetu Mkoa wa Simiyu na Mikoa ya Tabora, Mara na Mwanza, tunalima sana pamba, lakini pamba bado haina thamani kwa sababu hatutengenezi final products zinazotokana na pamba, isipokuwa tunafanya exportation ya material ambayo kule wenzetu wanakwenda kutengeneza final product.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeishauri Serikali, kuna andiko lilishaletwa Wizarani, Wizara ya Fedha na Wizara ya Viwanda, kujenga kiwanda Mkoa wa Simiyu ili uweze kuhudumia Mikoa ya jirani, na kiwanda hiki kitakuwa cha vifaatiba vitokanavyo na pamba. Tunajua tunaweza tukapata gozi, tunaweza tukapata mashuka. Tutaokoa fedha nyingi za kigeni ambazo tunakwenda kununua vifaa hivi nje, vitaendelea kupatikana kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kiwanda hiki pia kitatoa ajira kwa Watanzania, zaidi ya Watanzania 1,000 wataajiriwa kupitia viwanda hivi. Kwa hiyo tunapokuwa tunazungumza habari ya viwanda tunazungumza habari ya ku-maintain fedha yetu ili isiendelee kushuka thamani yake bali iendelee kupanda kwa kuwa na products ambazo zinapatikana kwenye nchi yetu. Mfano umeutoa, hata hivi vyuma ambavyo vinatengeneza reli tungekuwa tumetengeneza kupitia Liganga huko wataalam wanasema wala tusingekuwa na haja ya kuagiza. Maana yake fedha yetu ingeendelea kuimarika zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye kuimarika kwa fedha mimi huwa najifikiria swali moja, sijui wataalam wanasemaje, lakini huwa nawaza kwa nini mimi niko kwenye nchi yangu Tanzania ninakwenda hotelini naambiwa charge ni dola 200. Sasa nawaza kwa nini naambiwa dola 200 kwenye nchi yangu, si niambiwe tu laki nne ya Tanzania nijue? Kwa nini, kwa sababu demand ya dola itakuwa kubwa kuliko supply na demand ikiwa kubwa maana yake fedha yako ya Tanzania ina-depreciate.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najua wataalam haya wanashauri na mimi naomba niseme kama ambavyo amepiga marufuku Mheshimiwa Simbachawene hivi karibuni kutupa pesa chini wakati wa kutunza vikundi mbalimbali, kuna haja sasa Mheshimiwa Waziri kuja na sera ya kukataza charges zozote ambazo wana-charge katika fedha za kigeni. Hakuna sababu ya kwenda kwenye hoteli ukaambiwa dola, maana yake itabidi ukatafute dola ili uende ukalipe hiyo charge ambayo utakuwa umeambiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda siku moja pale…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Kabla ya taarifa, Wasukuma mtaipata, mlizoea kutupatupa hela chini sasa mtakamatwa wote. Taarifa inatokea upande gani? Mheshimiwa Ester.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa taarifa Kaka yangu, jirani yangu pale Mbunge wa Busega, kwamba ukienda nchi zingine ukifika airport lazima utabadilisha dola ili uweze kutumia kwa pesa za nchi husika, kwa hiyo ni jambo zuri.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa Mheshimiwa Lusengekile.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea kwa mikono miwili kwa sababu nilienda hoteli moja hapa Dar es Salaam nikanywa soda nikaambiwa dola moja, yaani nikawaza kwa nini naambiwa dola moja, si aniambie tu elfu mbili nijue. Lazima tuheshimu fedha yetu, tukiheshimu fedha yetu itakuwa na thamani, hakuna sababu ya ku- undermine fedha yetu. Mheshimiwa Waziri wa Fedha liangalie hili. (Makofi)

MWENYEKITI: Kwa hiyo Musukuma wewe unakwenda kwenye hoteli hujui hata malipo yatakuaje? Endelea mtani. (Kicheko)

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, issue hapa siyo kujua ni shilingi ngapi, issue hapa ni kuniambia anani-charge kwa dola hiyo ndiyo issue yangu. Mimi hata kama angesema 5,000 sina tatizo mtani, lakini shida ni kuni- charge kwa dola. Kwa hiyo, nataka tuimarishe shilingi yetu kwa namna ya pekee sana ya kuiheshimu fedha yetu. Mtu akifika airport pale ana dola zake atafute benki ilipo abadilishe achukue fedha zetu za ndani aende akaanze kutumia, hapo tutaimarisha shilingi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la riba, tumeona kwenye taarifa ya Kamati ya Bajeti. Wastani wa riba za mabenki kwenye kukopesha sekta binafsi tumeona ni asilimia 16.6. Ni kweli riba hizi ni kubwa na tunatamani mabenki yetu yapunguze riba.

MWENYEKITI: Kengele ya pili hiyo Mheshimiwa.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nami niungane na wachangiaji wengine kukupongeza kwa kuchaguliwa kwa kura nyingi sana. Naipongeza sana Kamati ya PAC na LAAC kwa taarifa ambayo wametuletea hapa inayoleta taswira kwa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ninaomba niishauri Serikali jambo moja. Serikali inapotaka kuingia kwenye uanzishwaji wa mifumo kwa ajili ya ukusanyaji wa fedha, naomba ifanye upembuzi yakinifu ili mifumo inayotengenezwa ije kuwa na tija kwa ajili ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Bandari mwaka 2010 iliingia mkataba wa miaka minne na Softech, mpaka 2014, kwa ajili ya kutengeneza mfumo wa ukusanyaji wa fedha. Mfumo huu ulikuwa unachukua gharama ya shilingi milioni 694, lakini mpaka kufikia mwaka 2014 mfumo haufanyi kazi na tayari Mkandarasi alikuwa amelipwa shilingi milioni 600 sawa na 87%. Inasikitisha kwa sababu fedha hizi ni za Watanzania, lakini mradi ule haukufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hawa Softech waliongezwa mkataba wa thamani ya shilingi milioni 55 kwa ajili ya kufundisha watumishi wa TPA ambapo mfumo haukufanya kazi. Pamoja na hayo, walilipwa shilngi milioni 55 zote na katika zile shilingi milioni 55 zilitakiwa kulipwa kwenye mkataba wa awali wa shilingi milioni 694. Serikali ikaingia hasara ya shilingi milioni 600 ya kwanza na ikaingia hasara ya shilingi milioni 55 ya pili. Hizi fedha ni za walipa kodi.

Mheshimiwa Spika, bado haitoshi, mwaka 2015/2016 kampuni ya 23rd Century System iliingia mkataba na Serikali ya kutengeneza mfumo pale TPA ambao ungegharimu shilingi bilioni 14, lakini mpaka mwaka 2019 mfumo huu haufanyi kazi, Serikali imelipa shilingi bilioni tisa; hasara kwa Serikali na hizi ni fedha za walipa kodi. Bado haitoshi fedha zililipwa shilingi bilioni tisa, lakini Mkandarasi hakulipa kodi ya zuio (Withholding Tax), akatoroka na fedha za wananchi sawa na shilingi milioni 874. Ni lazima Serikali ichukue tahadhari inapoanzisha mifumo ya ukusanyaji wa mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado haikutosha kampuni ya SAP mwaka 2020 ikaajiriwa; kazi yake ni kuangalia kama huyu 23rd Century System Limited alifanya kazi ambayo ilistahili kulipwa zile fedha. Naye akalipwa dola za Kimarekani 433,000 sawa na shilingi milioni 874. Hizi ni fedha za walipa kodi na bado mifumo haikufanya kazi. Tunavyozungumza sasa hivi, ule mfumo haukufanya kazi tena pale TPA na fedha za walipa kodi zililipwa. Katika mifumo hii ni shilingi bilioni 17 zilitumika na mfumo haukufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, siyo TPA peke yake, ukienda pale GPSA wamenunua mfumo wa shilingi bilioni 1,087, sasa wamekuja kugundua ule mfumo hautoi yale mahitaji ambayo walikuwa wanayahitaji. Wamekuja kugundua ule mfumo hautawasaidia tena. Sasa wameshindwa kuutumia ule mfumo na fedha za Serikali zililipwa shilingi bilioni 1,087. Wameandika kibali kwenda Wizara ya Fedha, wabadilishe watumie mfumo mwingine na Wizara ya Fedha imewakubalia na hasara tayari imepatikana katika fedha za walipa kodi. (Makofi)

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. HUMPHREY H. POLEPOLE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mzungumzaji anateremsha taarifa muhimu sana, nilitaka kumpa taarifa kwamba TANESCO mwaka jana 2021 mwishoni wameingia mkataba na kampuni ya kutoka India kwa zaidi ya shilingi bilioni 69 kwa ajili ya mifumo ya TEHAMA na watu wengi tunajiuliza kama uwezo huo wa kampuni kutoka India haupo nchini Tanzania licha ya kwamba mifumo mingine ya Kiserikali inatengenezwa hapa Tanzania?

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Simon Lusengekile unapokea taarifa hiyo.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, ninapokea taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tuone ni namna gani Serikali inaingia hasara katika mifumo ambayo haina tija na haileti matokeo chanya kwa Taifa. Wahasibu wanaita this is nugatory expenditure. The Government incur some expense that cannot generate economic benefit. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali kuchukua hatua za haraka kwa wale wote ambao wamesababisha hasara kwa Taifa. Watumishi ambao wapo ofisini wamesababisha hasara kwa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, tayari ameshaanza kuchukua hatua na kumwelekeza DG wa Bandari kuhakikisha kwamba wafanyakazi waliopo pale waliosababisha hasara hii wanachukuliwa hatua za haraka.

Mheshimiwa Spika, ninaishauri Serikali ichukue hatua kwa makampuni haya ambayo yalilipwa fedha nyingi na Serikali shilingi bilioni 17 na mfumo haukuleta tija ikiwepo na hii 23rd Century System Limited iweze kulipa fedha za TRA ambayo ilikuwa ni Withholding Tax, shilingi milioni 877. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo naomba pia nichangie kidogo kuhusu kiwanda cha sukari pale Mbigiri. Serikali iliingia mkataba wa kusimika kiwanda cha sukari cha kisasa pale Mbigiri, lakini mpaka sasa tunapozungumza, kiwanda kile hakijawahi kusimikwa na Serikali imepata hasara ya fedha kwa sababu walilima miwa wakijua kwamba kiwanda kitawahi kuja, miwa ile imeharibika, tayari Serikali imepata hasara ya zaidi ya shilingi milioni 300. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haitoshi…

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nampa taarifa jirani yangu wa Busega kwa mchango wake mzuri. Siyo Serikali tu, Mifuko ya Hifadhi ya Jamii imelazimishwa kuwekezwa hapo, PSSSF miaka mitatu imetengeneza hasara ya shilingi bilioni 11; na ukiuliza sababu, Serikali haijapeleka mashine.

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Simon Lusengekile, unapokea taarifa hiyo?

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, pale Mbigiri NSSF ina 96% na Magereza wana 4%, tunazidi kudidimiza taasisi zetu. Waliingia mkataba wa kununua miwa ya outgrowers; wakulima wa mazingira ya pale. Wakulima wamekopa fedha benki kwa ajili ya kuwekeza kwenye kilimo cha miwa wakijua kwamba baada ya kiwanda kuja watauza ile miwa. Kiwanda hakijasimikwa mpaka sasa hivi, wananchi wanateseka, wanashindwa kulipa mikopo kwa sababu kiwanda hakijapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Wizara husika sasa iharakishe kusimika kiwanda hiki ili kiweze kuleta tija kwa Watanzania. Ninaamini kitaleta ajira nyingi kwa Watanzania.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kunipa nafasi leo nichangie hotuba ya Waziri wa TAMISEMI. Kwanza nianze kumpongeza sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa sana anayoifanya katika Taifa letu. Amenikumbusha maneno ya Biblia, ukisoma Ezra 10 mstari wa 4 inasema: “inuka sasa maana kazi hii inakuhusu wewe; na sisi tu pamoja nawe; na uwe na moyo mkuu, ukaitende.”

Mheshimiwa Spika, haya maneno yananikumbusha kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais kwa sababu ameamua kuamka; ameinuka na kazi hii inamhusu yeye na ameenda kuitenda, nasi tuko pamoja naye kuhakikisha kwamba kazi inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI kaka yangu Mheshimiwa Innocent na wasaidizi wake wawili; Mheshimiwa Dugange pamoja na Mheshimiwa David, wanafanya kazi kubwa sana kwenye wizara hii ya TAMISEMI. Tunawapongeza kwa sababu tunaona matunda makubwa ya kazi ambayo mnafanya kwenye Majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampongeza sana Katibu Mkuu wa TAMISEMI, Profesa Shemdoe. Kwa kweli Profesa ni msikivu sana; tunapoenda sisi Wabunge na kazi zetu pale kwake anatusikiliza na hata ukimpigia simu anapokea wakati wowote, hata akiwa hana nafasi, anasema atapiga baadaye na kweli anafanya hivyo. Nampongeza sana, sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nampongeza sana Mkurugenzi Mkuu wa TARURA, kaka yangu Seif. Kwa kweli kaka huyu ni wa mfano sana kwetu; ni mtu anayesikiliza, ni mtu ambaye ukipeleka shida yako anatatua. Anawasiliana na watu wa wilaya kuhakikisha kwamba maeneo yetu yanakuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nami sasa nichangie kidogo kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, nianze na posho ya Madiwani. Nimezungumza na dada yangu hapa, nami naomba niseme kwamba Madiwani wanafanya kazi kubwa sana kwenye Majimbo yetu na kwenye Wilaya zetu. Ni watu ambao wanasimamia miradi yote ambayo inapelekwa na Serikali. Utamwona asubuhi Mheshimiwa Diwani anajikokota na baiskeli yake, anaenda kuangalia mradi umefikia wapi? Leo sisi kama Wabunge ni lazima tutafakari kwa maslahi mapana sana ya hao Waheshimiwa Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimekuja na hesabu ndogo hapa. Tuna Madiwani 5,287; ukiwapa tu posho yao hata shilingi 800,000/= kwa mwezi, tutakuwa tunawalipa kwa mwezi shilingi bilioni 4,200. Tuki-calculate hii kwa mwaka, tutawalipa shilingi bilioni 50.7. Ninaamini kwa Serikali yetu inawezekana kuwalipa kiasi hiki Madiwani ili waweze kufanya kazi nzuri kwa ajili ya Watanzania, kwani Madiwani wanafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, hata huko Mbeya najua wanakulindia Jimbo na wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba wewe unapokuwa hapa wao wanafanya kazi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba eneo linabaki kuwa salama. Kwa hiyo, niseme, sasa ni wakati muafaka wa Wizara kulichukua hili na kwenda kulifanyia kazi ili Madiwani wetu posho yao iimarike, nao hata wakienda Halmashauri kusimamia miradi, wawe na kitu ambacho wanaweza kujivunia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Madiwani wengi wanatumia baiskeli, kuna haya hapa mwanzoni wanapokuwa wameshinda watafutiwe hata mkopo wa bila riba, walau wapate pikipiki. Madiwani wanapoenda kusimamia miradi, wawe na usafiri ambao sasa ni chanya kwao kutembelea vijiji na Kata zao ili waweze kusimamia miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine naomba nizungumzie kidogo sehemu ya afya. Nimesoma Bajeti ya TAMISEMI, naishukuru sana Serikali kwa kutuletea vituo vya afya. Tuna kituo cha afya pale Busega tunajenga, Ngasamo, lakini kwa bajeti hii Waziri kwa kweli hajaweka kituo cha afya hata kimoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba Naibu Waziri wa TAMISEMI, kaka yangu, Mheshimiwa Dugange amekuwa Mganga Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, anaifahamu Kata ya Kabita. Hii ni Kata ya kimkakati yenye wapiga kura wengi sana. Ni Kata ya pili kwa wingi wa wapiga kura katika Jimbo la Busega. Ni muda muafaka sasa Serikali ione Kata hii ya mkakati kuipelekea kituo cha afya. Najua hatuwezi kujenga kila Kata lakini walau Kata za kimkakati tuweze kupata kituo cha afya. Nami ukiniuliza leo, nitakwambia kwa Jimbo la Busega kipaumbele kianze pale Kabita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, cha pili, kwenye Jimbo langu la Busega tuna maboma mengi ya zahanati wananchi wamejenga. Tuna zaidi ya maboma 15, lakini kwenye bajeti hii nimeona ukamilishaji wa maboma ya zahanati katika Jimbo la Busega imepangiwa zahanati moja ambayo itakamilishwa. Sasa kuna haja ya kuhakikisha kwamba tunaongeza walau tufanye kama ilivyokuwa mwaka wa fedha huu unaoisha tupate zahanati tatu ili tuweze kuzipunguza zile zahanati ambazo wananchi wameanzisha. Wananchi wanatumia gharama kubwa, wanajitoa kwa mioyo, muda mwingine hawapati chakula, wanahakikisha kwamba wanatoa michango kwa ajili ya kujenga zahanati. Sisi kama Serikali, kama wadau ambao wananchi wametuchagua, sasa tuweze kuwapangia fedha ili aweze kukamilisha zahanati zao. (Makofi)

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Simon Songe kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, anachokisema Mheshimiwa Mbunge wa Busega ni sahihi kabisa kwamba wananchi wamejenga majengo ya zahanati, vituo vya afya na madarasa ambayo wametumia nguvu zao na hata sasa yanashindwa kumaliziwa, nguvu za wananchi zinapotea bure. Ninavyosema hivyo Kituo cha Afya Msindo, Wilaya ya Namtumbo wananchi wamejenga jengo la upasuaji, mpaka sasa hivi bado hawajapata pesa ya kumalizia na jengo lile lipo kwenye hatari ya kudondoka katika msimu huu. (Makofi)

SPIKA: Ahsante sana. Mheshimiwa Lusengekile, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Spika, naipokea.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nataka nichangie ni eneo la TARURA. Pamoja na pongezi ambayo nimetoa kwa kaka yangu Seif lakini bado tuna kazi kubwa ni lazima tuongeze bajeti sasa eneo hili la TARURA ili tuweze kutengeneza barabara zetu. Vijijini bado kuna kazi kubwa ya barabara. Mfano, katika Jimbo la Busega tumetengeneza barabara za Kata zetu tatu lakini kwenye makutano ya zile barabara kuna tatizo la daraja pale Mwamigongwa.

Mheshimiwa Spika, sasa ni wakati sahihi kutafuta fedha zaidi ya milioni 500 twende tukatengeneze lile daraja ili tuwe na mawasiliano ya hizi Kata tatu, Kata ya Malili, Kata ya Imalamate na Kata ya Mkula pale kwenye makutano ili kata hizi ziweze kufunguliwa ili tuweze kusafirisha mazao na tuhakikishe kwamba wananachi wanasafirisha mazao yao yakiwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kuna barabara inayounganisha mikoa miwili, Mkoa wa Mwanza na Mkoa wa Simiyu. Barabara inayoanzia pale Sayaka inapita Nyaruande inapita Badugu inaenda mpaka Dutwa mpaka kule Bariadi. eneo hili pia tulitengee fedha ili tuweze kutengeneza kama ambavyo itakuwa imekusudiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo. naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma Kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie taarifa hizi za Kamati Tatu, nizipongeze sana Kamati kwa kazi kubwa ambazo zimefanya kutuletea taarifa ambayo inaenda kutufungua macho nini kinafanyika kwenye Kamati hizi Tatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa masikitiko makubwa sana katika taasisi zetu hizi mbili TANROADS pamoja na TAA katika muingiliano wa mamalaka ya utendaji wa kazi, kuna tatizo kubwa ambalo 2016 Mwezi Agosti ujenzi na upanuzi wa viwanja vya ndege ulihamishwa kutoka TAA kwenda TANROADS.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona matatizo makubwa viwanja wana-delay kufanya kazi lakini bado haitoshi wanaingiliana katika maamuzi. Nikupe mifano michache, mpaka sasahivi tunavyozungumza Kiwanja cha Ndege cha Shinyanga, Tabora, Sumbawanga hakijajengwa kwa sababu ya muingiliano wa majukumu kati ya TAA pamoja na TANROADS nini kilifanyika hapa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfadhili aliyekuwa anatuletea fedha kwa ajili ya ujenzi wa viwanja hivi alifanya due-diligence pamoja na TAA mwaka 2017 lakini baadae alivyotaka kuleta fedha akagundua kwamba tayari Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Vya Ndege umehama kutoka TAA kwenda TANROADS akakataa kuleta fedha na ujenzi haukuendelea, nini kilifanyika hapa? Wamekaa zaidi ya miezi 30 hamna kilichoendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais ameendelea na mazungumzo, mwaka jana Mwezi Februari, wameleta Dola za Kimarekani Million 12 kwa ajili ya Ujenzi wa Viwanja hivi, kwa masikitiko makubwa kwa sababu ya mwingiliano huu mpaka sasa hivi hakuna kinachoendelea na fedha zipo kwa Serikali yetu, ni masikitiko makubwa sana fedha hizi ni za mkopo walipa kodi watakuja kurudisha mkopo huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo mpaka sasa hamna kinachoendelea itafika sehemu tutalipa riba ya kutokutumia fedha ambazo zimekopeswa. Mpaka sasa hivi Mkandarasi aliyefanya quotations 2017 ameambiwa afanye implementations ya mradi naye amekataa amesema hawezi kwa sababu vitu vimepanda bei hawezi kufanya sasa hivi naye ameongeza bei. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wako ofisini wamekaa, watu wanajadili ofisini zaidi ya miezi 11 wako ofisini wameshindwa kutoa maamuzi kwa ajili ya ujenzi wa Kiwanja cha Ndege Shinyanga, Tabora na Sumbawanga. Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa sana katika Nchi yetu, lakini Watendaji wa Wizara wanamuangusha Rais kwa kutofanya maamuzi kwa wakati. Leo tuna Dola za Kimarekani Million 12 TANROADS hazijafanya kazi ni kwa sababu ya mwingiliano wa majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tunaomba sasa kama inawezekana tuamue kwa pamoja Wabunge turudishe Mamlaka ya Ujenzi wa Viwanja Ndege tutoe TANROADS tupeleke TAA ili kazi iweze kufanyika la sivyo tutakuwa tunazungumza viwanja havipanuliwi, hakuna kinachoweza kufanyika lakini mwingiliano huu utaona umetupa hasara ya Million 236 Kiwanja cha Ndege cha Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana walipanua wakaweka taa za solar kwa ajili ya kutua hizi ndege kubwa, lakini leo TAA zile taa ziliwekwa na TANROADS leo TAA wamekataa kwamba zile taa hazifai tena kwa sababu Mji wa Dodoma umepanuka sasa hawatatumia tena taa za solar wanaitaji taa za umeme Million 236 za walipa kodi zimepotea na sasa haiwezekani. Kwa nini? Kwasababu wanakati wanaweka hizi taa za solar hawakuwa na mawasiliano na kati ya TAA na TANROADS na fedha Million 236 za walipa kodi zimepotea kwa sababu ya Watendaji ambao hawana mawasiliano, hawawezi kufanya kazi zao kwa ajili ya kumsadia Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima leo tuwe na maamuzi ili tuweze kuisaidia Serikali, hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa Taifa hawa wote ambao wanasababisha hasara kwa nchi yetu wachukuliwe hatua ili iwe mifano kwa watu wengine kwa ajili ya kunusuru Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la pili ambalo nataka nichangie. Limechangiwa kidogo suala la riba katika miradi yetu. Leo nilikuwa natafakari hivi inawezekanaje Afisa Masuuli yeye anajisikiaje moyo wake anasaini vocha ya kupitisha malipo ya nyongeza ya kutokulipa kwa wakati kwa sababu amechelewa! Unapitisha voucher ya Milioni 100, unapitisha voucher ya Bilioni Moja unaenda kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa kumlipa Mkandarasi, haiwezekani leo Wabunge tuamue! Ni kwanini kila siku tunapiga kelele kwa sababu ya ucheleweshaji wa malipo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ikiwezekana Bunge hili liamue sasa Wizara ya Fedha ituletee taarifa ya kutupatia sababu kwa nini wanachelewa kulipa Malipo kwa Wakandarasi na kuleta riba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Daraja la Busisi wamechelewa siku 30 wamelipa riba ya milioni 58. TAA Bilioni 11 lakini Kiwanja cha Ndege cha Mwanza bilioni mbili. Sasa inawezekanaje Afisa Masuuli unasaini Vocha ya kulipa kwa sababu wewe mwenyewe ulichelewa na wewe uko ofisini haiwezekani! Ni lazima tutafakari tuisaidie nchi, ni lazima tutafakari tumsaidie Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais anafanya kazi kubwa, hawa Watendaji hawamsaidii. Leo Bunge tuamue ili tumsaidie Mheshimiwa Rais na wananchi wanamfurahia lakini kuna watu wanamuangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Naiba Spika, nizungumze kidogo kwa ajili ya mifuko hii ya wakopeshaji ya wajasiliamali wadogo wadogo. Tumeletewa taarifa kwenye Kamati tuna Mifuko 52 na ilikaguliwa Mifuko 13, lakini nimekuja kugundua katika mikopo waliyotoa bilioni 90 kati ya hiyo bilioni 90, bilioni 50 ni mikopo chechefu haiwezi kukusanyika, inawezekanaje?

Haiwezekani watu wanakopeshwa na mwisho wa siku hawarejeshi! Tumegundua kwa sababu, gani? Ni kwa sababu, wanakopeshwa watu ambao hawana sifa, inafika sehemu wanashindwa kurejesha mikopo ile. Sasa haiwezekani! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo la pili kwenye hii mifuko; wamekopesha zaidi ya asilimia 72 kwa benki za biashara, jambo ambalo si lengo la mifuko hii. Lengo kubwa la mifuko hii ni kukopesha wajasiriamali wadogowadogo, lakini tumekuja kugundua zaidi ya asilimia 70 zinakopeshwa benki ambayo si lengo la mifuko hii, tunayo ya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mifuko hii imetengenezwa ili iawasaidie wajasiriamali wadogowadogo kule vijijini, lakini hawapati mikopo kwa sababu wanaokopeshwa si wale wanufaika; na ndiyo maana sasa tunakuwa na mikopo chechefu kwa sababu watu wameacha malengo na makusudi ya ile mikopo wameenda kwenye malengo ambayo hawakupanga kuyafanya. Ukiona hivi maana yake hatukujiandaa katika hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tunayo mifuko mingi, 52, wote wanafanya kazi moja; na kwa sababu hawawasiliani, hamna sehemu wanaonana; leo Mheshimiwa Songe anakopa mfuko A, kesho akifulia kidogo anaenda kukopa B, keshokutwa akifulia kidogo anaenda kukopa C, mwisho wa siku anashindwa kurejesha.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tunaishauri Serikali, ifike mahali mifuko hii sasa iunganishwe iwe michache, badala ya 52 iwe hata minne ili iweze kuwasaidia wananchi wetu. Hata ikiwa inawezekana basi iweze kusomana ili kama umekopa sehemu A basi usipewe mkopo sehemu B, kwa sababu, hatimaye utashindwa kurejesha mikopo hii, ili iweze kuwasaidia wananchi wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili linatakiwa lichukuliwe hatua za haraka ili tuinusuru nchi yetu…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami nichangie hii Wizara yetu ya Maji. Kwanza nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna alivyotuletea fedha kwenye majimbo yetu kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maji iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee nimshukuru sana kaka yangu Waziri Aweso kwa kazi kubwa anayofanya ana sifa nyingi sana. Na hapa majuzi nimegundua sifa yake nyingine ambayo sikuwa naijua na ambayo inanifanya niendelee kumfagilia zaidi, nimekuja kugundua kumbe pia ni mshabiki wa simba. Kwa hiyo, ninazidi kukupongeza sana kwa kazi kubwa unayofanya na ni kweli tumeendelea kuona unavyoishi na misemo yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee pia, nimshukuru sana msaidizi wako, Dada yangu Mheshimiwa Injinia Maryprisca, Naibu Waziri wa Maji, anaupiga mwingi sana. Dada huyu sijui kama analala, lakini kwa kweli kazi kubwa anafanya. Nimemuona kwenye jimbo langu amefika tumetembea naye vijiji zaidi ya vinne, hakuchoka, hakula, ameenda kula jioni kule Bariadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimpongeze sana na nikuhakikishie kwamba, ulipofika pale Mkula ulisema ule mradi utafunguliwa hivi karibuni na kulikuwa na tatizo la pump, nikuhakikishie kwamba, pump imeshapatikana na wiki hii tulikuwa tunafanya water test na nina imani kwamba, mpaka mwisho wa mwezi mradi huu sasa wananchi wataanza kutumia maji pale kwa hiyo, nikushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kipekee pia, nimshukuru Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, kaka yangu Injinia Sanga. Anafanya kazi kubwa, anatusikiliza Wabunge, anatupa ahadi nzuri na ana ahadi pia amenipa nyingine, ninaomba aweze kufanya utekelezaji wake ndani ya mwaka husika wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru sana DG wa RUWASA kaka yangu Clement. DG anafanya kazi kubwa sana, upatikanaji wa maji vijijini; 2020 Jimbo la Busega upatikanaji wa maji ulikuwa asilimia 39, tunavyosema leo upatikanaji wa maji ni asilimia 64. Hizi ni jitihada kubwa sana za Mheshimiwa Waziri, jitihada kubwa sana za mkurugenzi wa RUWASA kwa kazi kubwa anayofanya kwenye majimbo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimshukuru dada yangu Mariam, Meneja wa RUWASA Mkoa wa Simiyu. Dada huyu anafanya kazi kubwa, anatuheshimisha sisi Wabunge na sisi tunasema tutampa ushirikiano kwa sababu yeye anatupa ushirikiano sana. Na niombe tu kama si namna ya kupanda basi msimuhamishe maana anafanya kazi kubwa, ila kama ni kupanda basi ruksa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nimpongeze kijana mwenzangu, Engineer Ngangari ambaye ni Meneja wa RUWASA Wilaya ya Busega. Ni kijana msikivu, anasikiliza, ananishauri na mimi ninamshauri mwisho wa siku tunatengeneza kitu ambacho ni kimoja kwa ajili yaw ana- Busega.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri, ni Mjumbe wa PAC. Tumeenda kutembelea miradi mbalimbali inayotekelezwa na mamlaka, wapo mameneja na wakurugenzi wa mamlaka husika wanafanya kazi kubwa kuhakikisha kwamba, wanasimamia miradi ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano; tulienda Dar-es- Salaam tukakutana na DG wa DAWASA, aisee, brother big up sana, DG wa DAWASA anafanya kazi kubwa na zaidi ya yote amesimamia hata mapato ya ndani kuhakikisha kwamba, anayapeleka kwenye miradi. Hiyo ni sehemu mojawapo ya kuiga kwa wakurugenzi wengine wa mamlaka, ili wanapopata fedha za ndani wapeleke kwenye miradi, lakini pia tumeenda kule AUWASA kule Arusha na kwenyewe wanafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeenda hapa Babati kwa kijana mdogo sana, Msuya, anafanya kazi kubwa sana kule Babati kwa ajili ya upatikanaji wa maji. Lakini Mkurugenzi wa MWAUWASA kule Mwanza anafanya kazi kubwa kwa ajili ya Watanzania wanaoishi pale Mwanza. Na sisi pia kwa mapato ya Wizara alitupatia mradi kule Busega kwa ajili ya kazi kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe mambo machache. Busega ndio kuna chanzo cha Ziwa Viktoria, lakini kuna vijiji ambavyo viko ndani ya kilometa 42 havina maji. Leo nikuombe, majuzi hapa ulijibu mradi wa maji wa Ziwa Viktoria kwenda Bariadi kutokea Busega, Maswa, Itilima na Meatu utaanza hivi karibuni. Niombe sana mradi huu ndio muarobaini wa matatizo ya maji katika Mkoa wa Simiyu, ndio muarobaini wa matatizo ya maji katika Jimbo la Busega. Nikuombe sana kama tayari umeshatangaza atakapopatikana mkandarasi basi aende kwa speed ili wananchi sasa walio wengi katika Mkoa wa Simiyu, hasa Wilaya ya Busega, waweze kupata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Mheshimiwa Waziri hivi karibuni mlitangaza mradi mkubwa wa maji pale Jimbo la Busega. Mradi wa thamani ya bilioni sita kwenye kata yetu ya Kabita, lakini mkandarasi hakupatikana, alikosa vigezo. Ninajua mnatangaza tena, niombe sasa speed iongezeke ili mkandarasi apatikane aweze kufanya kazi kwa ajili ya kuanza ule mradi. Nimeona kwenye bajeti tayari umetutengea, bajeti iliyopita milioni 950 na bajeti hii milioni 700. Ni imani yangu kwamba, ataanza kazi mapema ili wananchi waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pale Busega tuna kata kama tatu bado zina shida ya maji. Tuna Kata ya Nyaruhande, tuna Kata ya Igalukilo na Kata ya Ngasamo bado zina shida ya maji. Niombe sasa kata hizi tuziangalie kwa macho mawili ili tuweze kuzipatia maji na wananchi wa pale nao waweze kunufaika na Ziwa Viktoria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niunge mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Hotuba ya Waziri wa TAMISEMI. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anazofanya hasa katika utoaji wa fedha kwenye majimbo yetu. Tunamshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimshukuru sana Waziri wa TAMISEMI pamoja na wasaidizi wake na watumishi kwa ujumla katika Wizara ya TAMISEMI kwa kazi kubwa wanazofanya. Sisi tunapata faraja sana kwa kazi wanazofanya. Pia kipekee niipongeze na kuishukuru sana Timu ya Simba kwa kazi kubwa iliyofanya jana. Kwa kweli ilifanya kazi kubwa kwa ajili ya nchi na nchi imetulia kwa kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ina maana gani? Labda Mheshimiwa Waziri Jenista aiandike hii. Tuliwafunga Horoya goli saba na jana wamefungwa Yanga goli mbili jumla tisa. Maana yake nini? Magoli manne ni ya uongozi wa Mama kuelekea 2025, zawadi na magoli mengine matano ni zawadi ya Mama 2025 – 2030, ndiyo maana ya yale magoli. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Simon kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Rashid Abdallah Rashid.

T A A R I F A

MHE. RASHID ABDALLAH RASHID: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe mchangiaji taarifa kwamba asije kulalamika na muda. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Simon.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu ya Yanga ndiyo maana kasema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niende kwenye kuchangia. Pamoja na mambo mazuri ambayo yamefanywa na Serikali, pamoja na fedha ambayo tumepokea kwenye majimbo yetu sasa kuna mambo ambayo pia tunaomba kuiomba Serikali iweze kuyafaya ili tuweze kuwa na tija zaidi kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie eneo la afya. Katika Jimbo la Busega tuna vituo vya afya ambavyo vilipandishwa hadhi kutoka kwenye zahanati; Kituo cha Afya Kiloleli na Kituo cha Afya Lukungu kwa maana ya Lamadi. Vituo vya afya hivi bahati nzuri sana vilipandishwa na Dkt. Dugange akiwa RMO wa Mkoa wa Simiyu, anavijua vizuri, lakini mpaka sasa hivi havina wodi yoyote. Kwa mfano Lukungu tuna theatre pale, haifanyi kazi kwa sababu hamna wodi. Ukimfanyia mtu operation hamna pa kumpeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa Wizara ilione hili, vituo vya afya hivi viwili kwa maana ya Kiloleli pamoja na Lukungu kule Lamadi, viwekewe miundombinu ya majengo ili vianze sasa kufanya kazi kama vituo vya afya na kama vilivyopandishwa hadhi na Dkt. Dugange akiwa RMO kule Simiyu. Kwa hiyo anavifahamu vizuri kwa sababu yeye ndiye alivipandisha hadhi kutoka kwenye zahanati kwenda kwenye vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana tuyachukue haya kuwasaidia wananchi wa Kiloleli ili wapate majengo ya wodi kwa maana ya wodi ya wanaume, wodi ya watoto na wodi zingine pamoja na kule Lukungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo naomba nichangie eneo la TARURA. Najua kazi kubwa imefanywa na TARURA. Kazi kubwa tumefanya kwenye miundombinu ya barabara. Naomba nami nipige kura ya ndiyo kama Mheshimiwa Waziri atakubali, Engineer Seif awe mfanyakazi bora TARURA mwaka huu Mei, kwa sababu kwa kweli anatutia moyo sana kwenye majimbo yetu. Anafanya kazi kubwa, ukimpigia simu anapokea, ana-respond na fedha zinakuja kwa wakati na wakandarasi wanafanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niwaombe Mheshimiwa Waziri na ndugu yangu Seif, pale Busega tuna Daraja la Lutubiga kwenda Mwasamba, daraja ambalo linahitaji shilingi milioni 900. Tunaomba sana huruma ya Mheshimiwa Waziri tupate shilingi milioni 900 kwenye bajeti ya maendeleo ili tuweze kuwatengenezea daraja wananchi wanaotoka Lutubiga kwenda Mwasamba, kwa sababu imefikia sehemu sasa wanafunzi hawawezi kuvuka pale, imebidi tuwaombee kwenda kusoma kwenye kata nyingine ya jirani kwa sababu kile kijiji hakina mawasiliano na kijiji kingine cha Mwasamba. Kwa hiyo, tunaomba sana tupate shilingi milioni 900 za dharura ili tuweze kuwasaidia watoto wanapotoka Lutubiga kuelekea kule Mwasamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la tatu ambalo nataka nichangie, ni habari ya 20% za maendeleo kwenye mapato ya ndani kwenye halmashauri 56. Fedha hizi ambazo ni 20% katika mwaka wa fedha unaokuja ambao leo tunauzungumza hapa. Wamepanga 20% kwa baadhi ya halmashauri ambazo ziko 56 ikiwemo Busega, Bariadi DC, Bahi, Siha pamoja na zingine lakini jumla ziko 56. 10% ndiyo tunazopeleka kwenye maendeleo na 10% nyingine ni kwa ajili ya makundi maalum kwa maana vijana, wanawake pamoja na watu wenye ulemavu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana, hii 40% ilikuwa ni msaada sana kwenye halmashauri zetu kwa ajili ya mikakati na maendeleo ambayo tulikuwa tunafanya kupitia mapato ya ndani. Tunaomba waturudishie hizi fedha ili tuweze kufanya miradi ya kimkakati kwenye halmashauri zetu. Hii 10% haitatosha kufanya kazi za kimkakati kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Busega ni zaidi ya shilingi milioni 300 ambazo zimetolewa kwa ajili kupelekwa kwenye matumizi ya kawaida. Nimshawishi sana Mheshimiwa Waziri, hizi halmashauri tuzirudishie hizi fedha ili ziweze kufanya maendeleo. Kwa mfano, una shilingi milioni moja, sasa kwenye maendeleo tunaenda kupeleka shilingi laki moja. Kwa kweli kwa halmashauri zetu hizi haiwezekani na hizi ndiyo siasa zetu na hizi ndiyo zinazosaidia kazi za dharura kwenye majimbo yetu. Ikitokea kazi ya dharura fedha hizi ndiyo tunatumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, sisi kuna maboma mengi ambayo wananchi wamejenga, tukiwa na fedha hizi itatusaidia kupeleka kwenye miradi ya wananchi ambayo wananchi wetu wameanzisha. Kuna sehemu nyingine pia tunafikiria hata kuanzisha masoko ya kimkakati kutoka kwenye halmashauri. Fedha hizi wakitusaidia zitatusaidia kuweza kufanya kazi za kimkakati kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tumeona halmashauri hizi hazina fedha tuwaongezee OC ili waweze kupata fedha za kufanyia kazi za matumizi ya kawaida, lakini hizi fedha za maendeleo tunaomba zirudi 40%, 10% iende kwenye makundi maalum na 30% ibaki kwenye miradi ya kimkakati ili tuweze kufanya kazi kupitia majimbo yetu na kupitia fedha hizi. Tumwombe sana Mheshimiwa Waziri, atafakari tena pamoja na wasaidizi wake. Ikibidi kama inafaa waweze kuturudishia hizi fedha na kama wakiona haifai basi waturudishie za Busega ili tuweze kufanya kazi za kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna jambo ambalo pia limekuwa likizungumzwa hapa. Maboma ya wananchi na miradi ya kimkakati ambayo imeanzwa na wananchi. Wananchi wetu wana maboma mengi ambayo wameyaanzisha. Kwa mfano Busega tuna maboma 69 ya madarasa, tuna maboma 10 ya nyumba za Walimu. Wananchi wametoa fedha, wananchi wamejibana wameanzisha miradi hii, lakini bado iko kwenye maboma. Tumekuwa tukipata fedha tunapeleka kuanza miradi mipya. Tunaomba sasa TAMISEMI iangalie ifanye sensa nchi nzima ili kusudi tupate tupewe zaidi kwa ajili ya fedha za mkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami nichangie hotuba ya Wizara Maji. Kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anazozifanya katika kuhakikisha kwamba sehemu nyingi zinaanza kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimpongeze sana kaka yangu Mheshimiwa Aweso kwa kazi kubwa anazofanya, anayaishi yale maneno yake ambayo amekuwa akiyazungumza kila siku. Pongezi hizo ziende pia kwa Naibu Waziri kwa kazi wanazofanya pamoja na kwenye Ofisi ya Katibu Mkuu na wasaidizi wake. Kipekee nimpongeze sana Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA Bwana Clement kwa kazi kubwa anazofanya kuhakikisha kwamba anawasimamia mameneja wa mikoa na kuleta matokeo chanya kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee pia nimpongeze sana dada yetu Engineer Miriam Meneja wa Mkoa wa Simiyu kwa kazi kubwa anazofanya. Kwa kweli anatupa heshima kubwa sana kuhakikisha kwamba sehemu kubwa tunaendelea kupata maji pamoja na Meneja wangu wa Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa jambo kubwa alilofanya kuhakikisha kwamba wanaleta magari ya kuchimba visima katika mikoa yetu. Leo hapa naomba sasa nimwambie Mheshimiwa Waziri kwamba tumepokea gari katika Mkoa wa Simiyu tuneomba hizi gari sasa zikalete matokeo chanya kwa Watanzania. Tusinunue gari kuja kuzi-park, hakikisheni mnapanga bajeti kwa ajili ya kuendeleza gari hizi kwa ajili ya mitambo hii ambayo sasa tumeinunua na kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunapata fedha kwa ajili ya kuchimba visima. Tunataka wilaya zetu tuchimbe visima kwenye vijiji ambavyo nina shida ya maji. Kwa mfano pale Busega tunataka tuchimbe visima kwenye Kata za Shigala, Kata ya Igerukilo, Malili, Imalamate na Ngasamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tunaomba sasa gari hii itengewe bajeti ili iweze kufanya kazi. Kwa sasa tumeletewa lakini bado haijatengewa bajeti ya kuiendesha gari hii; na ili liende katika mikoa yote. Tutengenezee hivi sasa bajeti ili gari hzi ziweze kufanya kazi. Kila mkoa tupeleke bajeti kufanya kazi. Mfano tupeleke bajeti za mabomba na mafuta ili hizi gari sasa zilete tija kwa Watanzania na kwa kuleta tija ambayo Mheshimiwa Rais anaitaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie jambo moja ambalo kila siku tumekuwa tukipata ahadi hapa. Mradi mkubwa wa maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Mkoa wote wa Simiyu. Suluhisho kubwa Mheshimiwa Waziri hapa katika Mkoa wetu wa Simiyu ni mradi mkubwa wa Ziwa Victoria ambao utaanzia Busega, Bariadi, Itilima, Maswa na Meatu. Mradi huu ndilo suluhisho la maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi nimekaa hapa Bungeni mwaka huu ni wa tatu napitisha bajeti, kila mwaka mnaandika kilekile kwenye bajeti. Mwaka 2021/2022 mliandika kilekile, mradi huu utaanza mwaka huu na haukuanza. Lakini bado 2021/2022 mkaandika hivyo hivyo na haukuanza mradi huu. Sasa hivi nimesoma hapa mmeandika hivyo hivyo na mradi sujui kama utaanza. Ninaomba sasa tuchukulie maanani katika mradi huu uanze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikukumbushe, mimi nimeuliza maswali mawili hapa kwenye huu mradi; mwezi Aprili, 2021 niliuza swali nilijibiwa hivi naomba ninukuu majibu yalikuwa hivi kwenye huu mradi; “Mheshimiwa Spika, ujenzi wa mradi utaanza mwezi Agosti, 2021 na miji mikuu ya wilaya itakayonufaika ni Busega, Bariadi, Itilima Maswa na Meatu na vijiji vilivyoko pembezoni mwa bomba kuu umbaliwa kilomita 12 kila upande. Mradi huu umepangwa kutekelezwa kwa miaka minne.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ni miaka miwili imeshamalizika na huu mradi haujaanza. Sasa nini maana yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa hapa niliuliza mwezi Februari, 2022 swali hili hili kwenye mradi huu huu. Majibu yalikuwa hivi, ninanukuu; “Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Mbunge. Nikiri maelekezo ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ni kutumia rasilimali toshelevu ikiwemo moto pamoja na maziwa kuhakikisha kuwa matatizo ya maji yanamalizika. Tumepata fedha naomba nirudie hapa tumepata fedha bilioni 400 kwa ajili ya kutumia Ziwa Victoria na kutatua tatizo la maji Mkoa wa Simiyu ikiwemo Busega, Bariadi na Itilima. Kwa hiyo mkakati wa Serikali sasa hivi tupo hatua ya kumpata mkandarasi na tupo hatua za mwisho. Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge mkandarasi atapatikana mapema na kwa wakati ili utekelezaji wa mradi huu uanze mara moja.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ni mwaka na nusu nini maana yake? Lazima tuwe serious na kazi hii ambayo tunataka wananchi wetu tuone wanapata. Tunatamani wananchi wapate maji. Lakini bado, katika mwaka huu wa fedha inaandikwa tena hivi; ninanukuu; “Hadi mwezi Aprili 2023 kiasi cha shilingi bilioni 1.9 kimetumika kulipa fidia kwa wananchi. Aidha taratibu za kumpata mkandarasi kwa ajili ya ujenzi wa mradi zinaendelea na utekelezaji unatarajiwa kuanza katika mwaka 2023/2024”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii Habari ya mkandarasi itaisha lini? Kwa sababu kila mwaka ni mkandarasi kila mwaka ni mkandarasi Mheshimiwa Waziri mimi shilingi yako nakimbia nayo Busega, naomba kesho ukisimama utupe commitment ya Serikali kwenye huu mradi mkubwa wa maji wa Ziwa Victoria wa Mkoa wa Simiyu tunatamani wananchi wa Mkoa wa Simiyu tuondokane na tatizo la maji. Ni aibu leo kuzungumza Busega haina maji wakati kata ya mwisho kwa umbali ni kilometa 42 haiwezekani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa kuhitimisha kesho atupe commitment ya Serikali, haya maneno yaliyoandikwa hapa yaliandikwa 2021 yaliandikwa 2022 yameandikwa 2023 leo tunataka commitment ya Serikali ili wananchi wetu waweze kupata maji safi na salama kupitia Mradi wa Ziwa Victoria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo nataka nichangie kwa Wizara ya Maji ni kuhusu wakandarasi. Sasa hivi wakandarasi wanalaamika hawajalipwa fedha. Sasa ni muda ambao tunatakiwa tutafakari tunapoingia kufanya kazi na wakandarasi tuhakikishe kwamba fedha zipo, wanapo-raise certificate tuwalipe kwa wakati ili waweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi ni muda mrefu wakandarasi wetu wa miradi ya maji, miradi ya barabara hawajalipwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri aangalie wakandarasi wake awalipe ili waweze kufanya kazi, kwa sababu kama hawatalipwa kwa wakati, tuta-raise riba, tuta- raise kucheleweshwa kwa kazi za wakandarasi. Ili kazi za wakandarasi zimalizike kwa wakati na ili wananchi wanufaike na miradi hii, ni lazima miradi hii imalizike kwa wakati. Ikiwemo kuwalipa wakandarasi kwa wakati ili waweze kufanya kazi ambazo tumewapa. Bila kuwalipa kwa wakati kwanza kunawarudisha nyuma, kunachelewesha miradi, kunaongeza gharama za miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na–declare interest kwamba niko Kamati ya PAC, kila miradi inaongezeka gharama zake kwa sababu ya kuchelewesha kuwalipa na tatizo hili sasa limeanza. Wakandarasi huko site wanalalamika, wengine wameshafikisha asilimia 75 za miradi, asilimia 80 lakini wamesimama kwa sababu hawajalipwa fedha zao. Ni wakati muafaka sasa tuweze kuwalipa ili wafanye kazi ambazo tumewapa na kuwatuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa, maana bado nina muda dakika mbili naziona hapa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa muda wako umeisha.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami nichangie Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa namna anavyotafuta fursa za utalii na kuongeza utalii katika nchi yetu. Hongera sana Mheshimiwa Waziri pamoja na timu yako, Naibu Waziri kwa kazi ambazo mnafanya kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Wizara hii inaendelea kuwa salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo machache sana ambayo nataka nichangie leo. Mheshimiwa Waziri ulichokifanya Tarime sasa ni muda muafaka wa kuja kufanya vilevile kuwasikiliza wananchi wa Busega na wananchi wa Magu. Tuna Pori la Sayaka, umefanya kitu kikubwa sana pale Tarime, namna ulivyowasikiliza wananchi kwa kweli uliwapa faraja kubwa sana. Leo wananchi wa Busega na Magu wanataka waje wakusikilize, uwasikilize katika Pori la Sayaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Busega kwa maana ya Kata ya Nyaluhande kuna Kijiji kinaitwa Nyaluhande, Mamkala pamoja na Mwagindi. Vijiji hivi vilikuwa vinanufaika na sehemu ya eneo ambalo sasa limetafsirika kuwa ni pori. Wameendelea kulitumia zaidi ya miaka 40, wamelima zaidi ya miaka 40 maeneo yale, lakini sasa wamekuja kunyang’anywa na kuyafanya mapori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina tatizo na pori, na tunatamani na tuko tayari sisi wananchi wa Busega kufanya uhifadhi, kuhakikisha kwamba, mapori yanalindwa na hili pori lilindwe. Hata hivyo, kuna eneo la mita 840 wananchi wetu wamekuwa wakilihitaji siku zote, wamekuwa wakilitumia katika kazi ya kilimo, lakini sasa hawawezi kulitumia. Hivi karibuni viongozi wanawaambia limeni kwa mwaka huu, mwakani msilime, ufugaji nao umekuwa shida, wakipeleka mifugo wanakamatwa, wanataifishwa na wengine kuuzwa. Sasa ni wakati muafaka Mheshimiwa mchengerwa uje sasa uwasikilize wananchi wa jimbo la Busega na Magu, ili tuweze kujadili tatizo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi hapa nilikuwa nasikiliza hotuba ya Mheshimiwa Waziri katika suala zima la migogoro. Amezungumza pia kwamba migogoro inaongezeka kwa sababu pia wananchi wameongezeka. Nikawa najiuliza swali la kawaida kabisa, ni lini wananchi watapungua? Jibu unapata, hapana, hawatapungua kwa sababu tunaongezeka kila siku. Ukiangalia hata Sensa ya 2012, tulikuwa wananchi milioni 44, Sensa ya 2022 tuko milioni 61.7. Maana yake ni kwamba tumeongezeka kuwa watu 35 katika 1,000. Nini maana yake? kila mwaka wanaongezeka asilimia asilimia tatu. Sasa asilimia tatu ya milioni 61.7 maana yake katika miaka inayofuata kila mwaka watakuwa wanaongezeka watu milioni moja na laki nane. Sasa watu milioni moja na laki nane kwa miaka kumi ijayo tunategemea wataongezeka kuanzia milioni 15 mpaka milioni 20. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini maana yake? Mwaka 2032 tunategemea kuwa na watu milioni 75 mpaka milioni 80. Hii ni hesabu ya kawaida, haihitaji nguvu nyingi, inafahamika kulingana na sensa tuliyonayo na birth rate ya asilimia tatu ambayo imeonekana katika sensa ya mwaka 2022. Sasa mje na mpango kwa sababu watu hawatapungua. Njooni na mpango wa nini kifanyike kupunguza migogoro? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama itakuwa watu wanavyoongezeka na migogoro inaongezeka, maana yake wataongezeka 2023, 2024, na hata migogoro itaongezeka. Ni lazima sasa mje na mpango, ni kwa namna gani watu wataongezeka, lakini migogoro ipungue. Hiyo ndiyo mjenayo ili mweze kuona namna ya kutatua. Mkae Wizara ya Maliasili, Wizara ya Ardhi, Wizara ya TAMISEMI, mje na mpango wa pamoja ili mweze kutusaidia kuhakikisha kwamba wananchi wetu waweze kupata nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo nataka kuzungumza hapa ni suala la tembo na viboko. Sasa hivi limejitokeza la fisi, hususan katika moja ya kata huko Wilayani kwangu. Sasa ni wakati muafaka wa kuvuna baadhi ya viboko ili wananchi wetu waweze kupata nafuu, pale Jimboni Busega watu wamekufa, mwaka 2022 zaidi ya watu watatu wamekufa kwa sababu ya viboko. Ni wakati muafaka sasa mje mwavune ili wananchi wawe na amani katika yale mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inatakiwa kufanya research. Mfanye tu reseach kwa nini hili? Moja ya majibu mtakayoyapata ni kwamba wamezaliana sana. Watu tunaongezeka na wanyama wanazaliana. Sasa ifike muafaka wanyama tuwapunguze kwa sababu si hatujawatolea uzazi, kwa hiyo, tutakapowapunguza, wachache wataendelea kuzaliana. Kwa hiyo, watakapokuwa wanazaliana, wengine tunawapunguza. Tusipofanya hivyo, maana yake tatizo litaendelea kuwa kubwa, watu watakufa, watu watauawa na pia migogoro itaongezeka. Ni lazima pia baadhi ya wanyama kwa mfano tembo na viboko tuone namna ya kuwapunguza ili tuweze kuwa na tija. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka kuchangia hapa ni juu ya watalii na matumizi ya Uwanja wa Ndege wa Mwanza. Ukiangalia katika hali ya kawaida kutoka pale Mwanza kwenda Serengeti kwa maana ya lile geti ambalo liko pale Lamadi, ni kilometa chache, nafikiri ni kilometa 120. Sasa hapo ni karibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni lazima tuwekeze katika Uwanja wa Ndege wa Mwanza ili watalii wengine waanze sasa kushukia pia Mwanza ili nasi huku upande wa Kanda ya Ziwa tuweze kupata watalii. Watalii wataingilia huku kwenye geti la Serengeti ambalo liko Lamadi na wananchi wangu wa Lamadi na wenyewe watapata vipato kutokana na watalii watakaopita maeneo haya.nini maana yake? Watu watajenga hoteli, watapata ajira ambayo itatokana na watalii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ndugu yangu hapa Mheshimiwa Boniventura Kiswaga na wenyewe watajenga pale hoteli. Kwa ndugu yangu Mheshimiwa Mabula, hapa katikati nao watakuwa na hoteli pale. Hii itasaidia sana watalii wetu sasa kuongeza kipato katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine la mwisho, limezungumzwa hapa suala la Nyatwali. Kuna wananchi wangu ambao…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami kuchangia Wizara hii ya Fedha. Ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi anazoendelea kufanya pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa namna anavyoendelea kusimamia Wizara yetu ya Fedha na kuhakikisha kwamba Sera zinatekelezwa vizuri kwa ajili ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina jambo moja au mawili ambayo natamani kuyazungumza siku ya leo kuishauri hii Wizara. Kuna sehemu aliyochangia kaka yangu Mheshimiwa Mbunge wa Handeni, habari ya Kitengo cha Internal Audit katika Halmashauri zetu pia kwenye Wizara mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, bado kuna shida ipo kwenye kitengo hiki. Kwanza kabisa, lazima tufahamu kwamba bado kuna tatizo kubwa sana la uhuru. Wakaguzi wetu wa Ndani hawana uhuru kwa sababu wanaripoti moja kwa moja, sehemu kubwa wanawezeshwa na Maafisa Masuuli. Unakuta Afisa Masuuli huyo ndiyo anaeombwa gari kwa ajili ya Mkaguzi wa Ndani kwenda kufanya ukaguzi site. Akipenda anaweza akatoa gari, asipopenda anaweza asitoe gari, at the same time Mafungu bado yapo kwa Afisa Masuuli kwa sababu kazi hizi zinafanywa na mapato ya ndani lakini pia na mapato ya OC kutoka Serikali Kuu. Sasa hapa uhuru lazima ukosekane. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimshauri Mheshimiwa Waziri sasa, kuhakikisha kwamba wanatengeneza vote, mwaka jana tulipitisha hapa tukakubaliana kwamba watengeneze vote kwa ajili ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani ili aweze kupeleka rasilimali huku chini kwa Wakaguzi wa Ndani wa Halmashauri lakini Wakaguzi wa Ndani wa Wizara mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nini kitakachopatikana hapa? Wakaguzi wa Ndani watakuwa na uhuru wa kufanya kazi zao bila kumtegemea Afisa Masuuli. Afisa Masuuli atakuwa anapewa taarifa za kiukaguzi kama Meneja wa sehemu husika kwa sababu ndiye anayetakiwa kujibu zile hoja za Mkaguzi wa Ndani. Tukilifanya hilo tutawapa uhuru mkubwa kwa sababu sasa hivi hawana uhuru wa kusema wakati wanatekeleza majukumu yao ya ukaguzi wa fedha zetu ambazo tunapeleka fedha nyingi kwenye Halmashauri na tunapeleka fedha nyingi kwenye Wizara zetu lakini Wakaguzi hawa wa Ndani hawana ule uhuru wa kutekeleza majukumu yao kwa sababu Maafisa Masuuli ndiyo wanaowawezesha kutekeleza yale majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hawawezi kufanya kwa sababu Afisa Masuuli huyo huyo unamwandikia kwenda kukagua mradi wakati anajua mradi huo una matatizo, atakuchenga wala hatakupatia fedha kwa ajili ya kutekeleza majukumu hayo. Fedha zitoke moja kwa moja kwa Vote ya Mkaguzi Mkuu wa Ndani zishuke chini ili waweze kufanya kazi kwa uhuru mkubwa na tutaweza kuona matokeo ya kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tuziimarishe hizi Kamati za Ukaguzi za taasisi husika. Mheshimiwa Waziri, kuna sehemu nyingine hata hizi Kamati hazipo, kuna baadhi ya Halmashauri hata hizi Kamati hazipo, hazijaundwa. Ukisoma Public Finance Act ya Mwaka 2010 Cap. 348 inaeleza vizuri kabisa lakini kuna baadhi ya sehemu Kamati hizi hazipo, sasa ufanisi wao unakosekana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili ufanisi wao upatikane ni lazima pia mzifuatilie Kamati hizi na kuona kama zinafanya kazi. Vilevile, nazo pia bado zinakumbwa na tatizo la uhuru kwa sababu Kamati zinategemea posho kutoka kwa Afisa Masuuli, ni lazima tutengeneze vizuri hapa ili tuweze kufanya vizuri zaidi kwa ajili ya hizi Kamati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni rasilimali watu. Bado Wakaguzi wa Ndani ni wachache, ongezeni Wakaguzi wa Ndani kwenye Taasisi za Serikali ili tuweze kupata ufanisi wa kazi ambazo wao wanazifanya. Unakuta kwenye Halmashauri kuna Mkaguzi wa Ndani mmoja lakini kazi ziko nyingi, atafanyaje kuhakikisha kwamba hizi kazi zinafanyika na kudhibiti huu ubadhirifu unaoendelea katika kazi zao? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho nimekiona na kimekuwa kikija kwenye Kamati na nimekiona ni kizuri ambacho kinafanywa na CAG na tunatamani pia kifanywe na Idara hii ya Ukaguzi wa Ndani, ni zile kaguzi za performance audit (Value for money) lakini pia real time audit. Kaguzi hizi zikifanyika kwa wakaguzi wa ndani zitatusaidia pia kuhakikisha kwamba tunalinada rasilimali zetu tulizo nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa ninataka kuomba nini? Mheshimiwa Waziri sasa ni lazima mfikirie kuajiri professionals nyingine zaidi ya professional za kihasibu katika hizi kaguzi zetu za ndani, lazima pia tuwe na Engineers kwenye Idara ya Ukaguzi wa Ndani ili anapokwenda kukagua miradi awe anajua anakwenda kufanya nini, kwa sababu kinachofanyika sasa hivi Mkaguzi wa Ndani ni Mhasibu anakwenda kukagua kwenye jengo fulani, anapokuwa anafanya kazi za value for money, inabidi sasa kwa sababu anakuwa hajui chochote kuhusu Engineering amuulize Engineer wa halmashauri kwamba hivi ilitakiwa kuwa nondo ngapi? Wakati huyo Engineer ndiye mkaguliwa! Sasa hii haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lazima tuweke professional zingine kwa hiki kitengo cha internal audit ili kiweze kufanya kazi vizuri. Vilevile Mheshimiwa Waziri tuwape mafunzo. Mambo yanabadilika lakini bado hatuwapi mafunzo. Tuwape mafunzo Wakaguzi wa Ndani, Wahasibu wa Halmashauri na Wahasibu wa Taasisi zetu ili waweze kufanya kazi sawa sawa na miongozo mipya pamoja na miongozo ya kiuhasibu inayotoka ili watekeleze majukumu yao vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unakuta Mhasibu yuko Halmashuri miaka 15 anaandika voucher, voucher kila siku halafu unaita tuna Mhasibu! Hapana. Uhasibu siyo kuandika voucher tu peke yake, afanye na majukumu mengine. Mpelekeni kwenye training, mpelekeni kwenye mafunzo ili ajue ni mabadiliko yapi ya kiuhasibu ambayo yanatokea katika miaka mbalimbali ya fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano ukiangalia kama sikosei ni mwaka 2022 au 2021 kuna mabadiliko ya hizi IPSAS, Hisa na vitu vingine lakini ukuwauliza wale Wahasibu walioko kwenye Halmashauri na walioko kwenye Wizara kuna wengine hawajui kabisa kama kuna mabadiliko lakini mabadiliko yapo. Unakuta kuna mabadiliko ya watu kusaini, kuna mabadiliko mbalimbali ya kifedha lakini wao wanatengeneza vitabu vyao vya hesabu ukilinganisha na sera zilizokuwepo toka mwanzo bila kufuata mabadiliko ambayo yametokea hivi karibuni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri nikuombe tenga fungu kwa ajili ya mafunzo kwa Internal Auditors, tenga fungu kwa ajili ya mafunzo kwa Wahasibu ili waweze kuendana na kasi ambayo inatakiwa na kuweza kufanya kazi katika nchi yetu na kazi zenye ufanisi. Tunataka kuona kazi zenye ufanisi katika Halmashauri zetu, tunataka kuona kazi za ufanisi katika Wizara zetu ili tumrahisishie CAG, muda mwingine tunampa CAG kazi kubwa bila sababu wakati kuna Wakaguzi wa Ndani. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo ninaomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. SIMON S. LUSENGEKILE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami kuchangia hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri. Nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa bajeti nzuri sana ambayo ametuletea mwaka huu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri wakati anatoa hotuba yake kuna sehemu nyingi sana alizoelekeza na alizosema za kupunguza matumizi, lakini kuna sehemu moja ambayo hakuitaja ambayo naona ni ya muhimu sana ya kupunguza matumizi katika nchi yetu. Eneo hili ni kupunguza matumizi ya Serikali ya eneo la riba na faini ambazo inatozwa Serikali kutokana na ucheleweshwaji wa malipo kwa wakandarasi na wazabuni. Eneo hili ni eneo muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakandarasi wana charge interest kwa Serikali kwa sababu tumechelewesha kuwalipa. Kama hatutabana hii sehemu, maana yake tutaendelea kuiingizia Serikali hasara, tunaendelea kupandisha miradi thamani yake, lakini pamoja na hayo, Serikali inazidi kupata hasara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe mifano. Ukisoma ripoti ya CAG ya mwaka wa fedha 2020/2021 iliyotolewa Machi 22, inaeleza; ukisoma ukurasa wa 52 na 53 wa Hesabu za Mashirika ya Umma, utaona tulichajiwa interest na faini ya Shilingi bilioni 95.2 ambapo TANESCO ilikuwa shilingi bilioni 10.4, ATCL ilikuwa shilingi bilioni 16.8 na Bodi ya Mikopo ilikuwa shilingi bilioni 68. Fedha hizi ni nyingi kwa Serikali. Ukienda kwenye Hesabu ya Serikali Kuu, utakuta TANROADS walichajiwa shilingi bilioni 68.7 na TARURA walichajiwa shilingi bilioni 0.88 sawa na shilingi milioni 880. Fedha hizi ni nyingi, lazima twende tukaziokoe.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba sasa Wizara kutazama kwa kina Hazina ili kuweza kutoa mlolongo uliopo mkubwa katika namna kubwa sana ya ku-approval malipo kwa Wakandarasi wetu. Tuki-solve hili eneo tutaokoa fedha nyingi sana kwa Taifa letu, tutaokoa fedha nyingi sana kwa nchi yetu. Namaanisha nini? Ukienda kwa mfano, Kamati yetu ilienda pale TPA tukakuta wamepigwa faini ya kuchelewa kulipa, ya shilingi milioni 980. Fedha hizi ni nyingi, lakini ukiuliza sababu utaambiwa kwamba Hazina ilichelewesha malipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia, tunapata mikopo ya watu wa Benki ya Dunia, tunaposaini mikataba, yaani financial agreement, Benki ya Dunia huwa inaleta fedha zote inazipeleka Hazina. Sasa kigugumizi cha kulipa Wakandarasi kinatoka wapi? Kwa nini hatuwezi kulipa wakandarasi kwa wakati ili kuondoa hii gharama ya kulipa interest? Implication yake ni nini katika hili?

Mheshimiwa Naibu Spika, implication yake ni kwamba inawezekana kuna viongozi kwenye ofisi wanachelewesha kwa makusudi ili watakapotoa fedha hizi waweze kupata mgawo. Hii ndiyo implication ya tatizo hili. Implication ya pili, Wakandarasi wameshatugundua sasa kwamba Watanzania wao hawalipi kwa wakati, tutachaji interest. Kinachofanyika sasa wanapofanya quotation ya kazi wana-quote kidogo wakijua kwamba watakuja wafidie pale kwenye interest.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili ni muhimu sana Wizara ya Fedha kuliangalia. Nendeni pale Hazina, kama kuna issue zinasumbua, fumueni utaratibu, leteni tuwapitishie hapa, tuokoe fedha nyingi ambazo tunaingia gharama bila sababu za msingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili ambalo nataka kuchangia, ni kuimarisha mashirika ya Serikali yanayozalisha na kupata kipato.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuchukulie mfano Shirika letu la TPDC, katika uagizaji wa mafuta mwezi Mei, 2022 mafuta yaliyoingia nchini ya diesel yalikuwa metric ton 346,631. Katika hii Shirika letu la TPDC lilipewa metric ton 111,000 sawa na asilimia 32, ukiuliza wanakuambia hawana mtaji! Leo lazima tukubaliane tupeleke mtaji katika Shirika letu ili liweze kuagiza mafuta mengi na tuweze kupata faida Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukisoma taarifa ya fedha utaona kwamba tayari wameshapleka gawio Serikalini zaidi ya Bilioni Tisa katika miaka mitatu, sasa kama hatuwezi kuwapelekea mtaji watapata wapi gawio la kuleta Serikalini ni lazima sasa tuone namna ya kuwapa fedha ili waweze kufanya biashara na tuweze kupata gawio Serikalini. Haya ni mambo ya msingi yatakayoenda kutupatia fedha katika nchi hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo ukiangalia kuanzia 2004 Julai, mpaka Mei, 2022 TPDC wameokoa Trilioni 41 wa kutumia gesi asilia, lakini ukisoma taarifa inaonesha mpaka sasa hivi wanaotumia gesi asilia ni asilimia 10 bado asilimia ni ndogo sana. Kama tumeweza kuokoa Trilioni 41.3 sasa haya si ni mahesabu tu ya kawaida comrade Mwigulu, kwamba sasa tupeleke fedha nyingi TPDC ili tuweze kuokoa fedha nyingi na baadae tupeleke fedha kwenye mzunguko ndiyo logic ya hii Habari! Kwa hiyo tulione suala hili ni la msingi sana, kama tumeokoa Trilioni 41 na bado ni asilimia 10, Je, tutaokoa kiasi gani kama tutafikisha asilimia 60 hii ni hesabu ya kawaida twendeni tukaliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala langu la Tatu ni kuangalia sekta za uzalishaji. Ninaipongeza sana Serikali kwa kuja na mkakati wa sekta ya kilimo kwa ajili ya uzalishaji. Niseme tu kwamba sababu mojawapo inayosababisha ongezeko la bei kwenye bidhaa mbalimbali ni kutokuwepo uzalishaji mkubwa wa mazao ya nchi husika. Tusipozalisha kwa wingi hapa nchini maana yake bei za mazao zitaendelea kuwa kubwa kwa sababu tunategemea kuingiza kutoka nje. Nini kifanyike, tunatakiwa tuzalishe kwa wingi hapa nchini ili tuweze nasi kuuza kwa wenzetu, tukienda mbali zaidi tuweze kutumia hapa nchini kwetu tuzalishe final product na hizi final product zikaweze kutumika katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano kule Simiyu tunalima sana pamba lakini tunalo andiko kubwa ambalo limekuja Wizara ya Fedha la kutengeneza kiwanda kikubwa Simiyu kitakachozalisha vifaa tiba vitokanavyo na pamba. Vifaa tiba hivi vinaenda kuokoa fedha zaidi ya Bilioni 147 ambayo tunatumia sasa kuagiza vifaa tiba huko nje. Sasa kwa nini tusizalishe hapa tutengeneze kiwanda, tuzalishe sisi wenyewe na tutumie, hii itaokoa fedha nyingi ambazo tunapeleka kule nje. Pia zaidi ya wananchi 1,000 wanaenda kupata ajira, kule Busega watapata ajira, kule Bariadi watapata ajira, kule Iramba watapata ajira. Kinachotakiwa sasa kufanyika ni kuwekeza eneo hili ili wananchi wetu waweze kupata ajira na tuokoe fedha nyingi katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii ndiyo itakuwa sasa mantiki ya kuwepo kwa reli, huwa najiuliza swali moja huko nyuma kwamba kwa nini tunajenga reli wakati hatujaenda kuwekeza katika sekta za uzalishaji, hii reli inaenda kusafirisha nini? Lazima tuwe na mipango, reli siyo ya kusafirisha watu peke yake, reli ni ya kusafirisha pia mizigo ya kusafirisha mazao. Mantiki ya kutengeneza reli ni pamoja na usafirishaji kama tunatengeneza reli kwa ajili ya kusafirisha watu hatutarudisha huo mkopo. Ni lazima sasa twende mbali zaidi tunatengeneza reli na mwisho wa siku huko reli inakoenda kuna uzalishaji gani. Kama reli inaenda Mwanza kuna uzalishaji gani kule Mwanza, kama reli inaenda Kigoma kuna uzalishaji upi kule Kigoma ambao sasa tutatumia katika suala zima la usafirishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)