Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Justin Lazaro Nyamoga (30 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, pia nami nitumie fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ananiwezesha kwa mara ya kwanza kusimama hapa Bungeni na kuchangia. Nikushukuru wewe, lakini pia niwashukuru wananchi wa Jimbo la Kilolo ambao waliniamini na kunituma niwawakilishe.

Mheshimiwa Spika, nitajielekeza kwenye suala zima la kilimo na mnyororo wa thamani, lakini kabla sijaenda huko, napenda kupongeza na kuunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais ambayo ilijaa hekima, busara, mwongozo na maono ambayo naamini katika miaka mitano ijayo tutakuwa na story au hadhithi ya kusimulia ya mabadiliko.

Mheshimiwa Spika, pia niipongeze Tume ya Uchaguzi, kwenye hotuba ilionesha wazi kwamba walifanya matumizi mazuri ya hela hadi kuwa na albaki ya karibu bilioni 69, kiwango cha uadilifu mkubwa ambacho walikionesha.

Mheshimiwa Spika, tukielekeza macho yetu kwenye suala zima la kilimo hasa kwenye suala la uwekezaji, napongeza hotuba hiyo kwa sababu ukurasa wa 29 unataja chai pamoja na mazao mengine kuwa mazao ya kipaumbele. Naomba nijikite kwenye hili suala la chai hasa mawazo na maoni ya wananchi wa Kilolo.

Mheshimiwa Spika, pale Kilolo kuna jumla ya hekta 3,600 ambazo zina rutuba kwa ajili ya kilimo cha chai. Siyo hivyo tu, kuna zaidi ya hekta 184 zimepandwa chai tangu miaka ya 1990 na kuwekewa kiwanda feki. Ile michai hivi tunavyozungumza, ile miti imekuwa inatosha hata kujinyongea. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, tangu miaka ya 1990 imekuwa ni kutafuta mwekezaji. Sasa najiuliza, pamoja na nia na dhamira ya Mheshimiwa Rais, ikiwa tutachukua zaidi ya miaka 30 kutafuta mwekezaji kwa ajili ya shamba na kiwanda cha chai kimoja, tutafika ndani ya miaka mitano?

Mheshimiwa Spika, lazima kuna mahali tunakwama. Nami napenda sana kumwomba kaka yangu, Waziri anayehusika na uwekezaji pamoja na viwanda na biashara ambao wanalijua jambo hili walitilie mkazo kwa sababu uzalishaji wa chai katika Wilaya ya Kilolo ambapo ardhi yake inafanana na Wilaya ya Mufindi yenye zaidi ya viwanda saba, hiyo ingeweza kukuza uchumi kwa kiwango kikubwa na wananchi wale waliopanda ile michai wanataka kuanza kung’oa kubadilisha mazao.

Mheshimiwa Spika, napenda kulizungumzia hili kwa mkazo kwa sababu watu ni lazima wajue kwamba moja ya sababu ya kupanda ile chai ilikuwa ni zao linaloweza kulinda vyanzo vya maji ambayo ndiyo yanayoenda Mtera na hata Kidatu. Kwa hiyo, tutakapobadilisha na kulima zao lingine pia tutavuruga vile vyanzo vya maji ambavyo vinalindwa kutokana na kulima lile zao la chai.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili, nizungumzie zaidi kuhusu tafiti zinazofanywa na uelekezaji wa mazao. Hivi karibuni nilimwona Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa kule Kigoma akihimiza sana utafiti wa mbegu na uzalishaji wa zao la mchikichi ambalo linalimwa katika mkoa ule.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa kwamba watu wa Kilolo wanalima maparachichi; na siyo Kilolo tu, ni Mkoa mzima wa Iringa na sehemu ya Mkoa wa Njombe. Changamoto yake ni aina ya miche wanayopanda, hiyo mbegu wanayolima; je, ni ile ambayo itapata soko wakati watakapoanza kuvuna?

Mheshimiwa Spika, hapa napenda kutoa ushauri kwamba ipo hii Taasisi ya Utafiti inayoitwa TARI, napenda waelekeze nguvu kwenye utafiti wa mazao ya matunda na mbogamboga kwa kuweka kituo kabisa katika Mkoa wa Iringa au Njombe kwa ajili ya kuhakikisha haya mazao kama parachichi yanapolimwa, wakulima wanalima mazao sahihi ambayo yatapata soko wakati wa kuvuna utakapofika.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kila mtu anakuza miche, anaokota mbegu huko, wakulima wanauziwa, wakati mwingine wanaambiwa ndani ya miaka mitatu wataanza kuvuna, ikifika miaka mitatu mti unarefuka tu na hakuna mazao kwa sababu hawakujua kama hiyo mbegu wanayotaka kuilima ni bora ama siyo bora. Udhibiti wa mbegu hasa miche, ni changamoto kwenye uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kuzungumzia umuhimu wa mnyonyoro wa thamani katika mazao yanayolimwa kwenye maeneo yetu. Kwa sababu tuna nia ya kuwa na nchi ya viwanda, ni lazima kuangalia ni jinsi gani tunaboresha mnyororo wa thamani. Nitatoa mfano wa zao la nyanya ambalo linalimwa sana katika baadhi ya maeneo kwenye Jimbo langu pia. Maeneo hayo ni Ilula na Ruaha Mbuyuni yote ambapo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa huwa wanapita na kununua nyanya.

Mheshimiwa Spika, wakati unapita mara ya kwanza unaweza ukanunua tenga moja kwa shilingi 10,000/= lakini upo wakati utakaonunua kwa shilingi 90,000/=. Sababu ni kwamba hakuna namna nzuri ya uongezaji wa thamani kwa mazao yetu. Kwa hiyo, wakati fulani wananchi wanalima kwa gharama kubwa na wanashindwa kuvuna na kuuza kwa bei kubwa kwa sababu thamani yake haijaongezwa.

Mheshimiwa Spika, nafikiri haujafanyika utafiti wa kutosha wa masoko kwa sababu nafahamu ziko nchi ambazo hazilimi nyanya lakini zinauza nje. Wakati mwingine tumesikia baadhi ya mazao yanasafirishwa kwenda nchi nyingine na kule yanapofika ndipo yanapouzwa. Mfano mmojawapo ni parachichi; ukifanya utafiti utakuta bandari zetu bado hazi- pack na kupeleka nje, wala viwanja vyetu vya ndege; lakini zipo nchi ambazo tayari zinafanya hivyo kwa kuchukua mazao hayo kutoka kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, hili tusipolifanyia kazi maana yake ni kwamba tunazinufaisha hizo nchi jirani. Pamoja na ujirani mwema, lakini siyo kwa kufikia kiwango cha sisi kulima parachichi, miti ya mbao, zikauzwe kupitia nchi jirani. Napendekeza suala hili lifanyiwe utafiti wa kutosha na Wizara zinazohusika ili mazao yanayolimwa na wakulima kwenye maeneo yetu yaweze kuongezewa thamani na wananchi wale waendelee kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia ukurasa wa 33 unaoelezea kuhusu ubora wa mifugo na vitu vingine mbalimbali. Tukizungumzia mifugo, tunazungumzia uboreshaji wa thamani. Katika hili napenda kupongeza maana ndani ya hotuba hii imetaja baadhi ya machinjio yanayoboreshwa. Katika Mkoa wa Iringa iko machinjio moja ambayo naamini ni mojawapo itakayoboreshwa.

Kwa kuwa machinjio hizi baadhi yake zimechukua muda mrefu; na kwa kuwa baadhi ya watu wanaoishi katika maeneo yetu ya Jimbo la Kilolo na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa ni wafugaji, napendekeza kasi ya uboreshaji wa machinjio hizi iweze kuwa ya kwenda mbele ili wananchi hao waweze kufaidika mapema.

Mheshimiwa Spika, wakati huu ninapozungumzia hili, napenda pia nizungumzie kuhusu vyanzo vya utalii hasa katika Mkoa wa Iringa na hususan Jimbo la Kilolo ambalo natoka. Moja kati ya utalii unaohimizwa ni utalii wa kihistoria. Pale kwenye Jimbo langu la Kilolo, Kihesa Mgagao pale waliishi wapigania uhuru wa maeneo mbalimbali, hata Rais Mstaafu wa Afrika Kusini, Marehemu Nelson Mandela alishafika pale. Pia pana kumbukumbu nyingi za wapigania uhuru hao, kumbukumbu ambazo kwa sasa lile eneo limegeuzwa kuwa gereza.

Mheshimiwa Spika, sisi wananchi wa Kilolo hatusemi kwamba hatufanyi makosa; tunafanya, lakini gereza lile idadi ya wafungwa wake hawafiki 20. Pia pale ni sehemu ya kumbukumbu za kihistoria. Wanafunzi wa Kilolo na maeneo mengine ya Mkoa wa Iringa hawawezi kwenda kujifunza pale kwa sababu ya ulinzi uliowekwa mahali pale.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo yote, napenda kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi hii. Nimepitia Mpango huu na ningependa kuchangia kwenye mambo machache kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu mfumo wa kodi hasa kwa wafanyabiashara wa mazao mbalimbali ya misitu na mazao ya mbogamboga. Sheria ya kodi hii inamtaka kila mfanyabiashara mwenye mzunguko unaofikia shilingi milioni 14 basi awe na mashine ya EFD na kwa hiyo, haikuzingatia baadhi ya vitu ambavyo vinawakwaza wafanyabiashara. Nitoe mfano kidogo kwamba, wako watu ambao wanauza mara moja tu, kwa mfano wakulima wa miti ya mbao anachana mbao na anauza anaweza akapata milioni 30 na akapeleka mzigo wake au wafanyabiashara wa mazao wanaonunua kidogokidogo na mzigo unafika kwa kiwango hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kuna utaratibu wa mageti ambapo yule mwenye mzigo akifika pale, basi anadaiwa risiti ya mahali alikonunua. Hii inatakiwa kurekebishwa kwa sababu kwa kufanya hivyo inawataka watu wengi sana ambao ni wakulima wa kawaida, watu wengi sana ambao ni wafanyabiashara wa mara moja, huo mzunguko wanaupata kwa haraka na sidhani kama tuko tayari kugawa mashine za EFD kwa wakulima, tuko tayari kugawa mashine za EFD kwa mtu anayechana mbao mara moja tu akauza. Irekebishwe ili iseme wafanyabiashara wa maduka au wafanyabiashara wenye sehemu ya kudumu kwa sababu, ndiko ilikolenga, lakini haiku-specify kwa hiyo, wale wa TRA wanapojaribu ku-execute wanasababisha usumbufu kwa baadhi ya wafanyabiashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kuzungumza ni ujenzi wa viwanda vya kimkakati. Juzi hapa nilitembelea kiwanda kimoja cha kutengeneza samani na kimejengwa na VETA kiko hapa Dodoma. Nikajiuliza sababu, iliyofanya VETA kujenga kiwanda hapa kwa sababu, ni cha samani; sikuona kama kuna misitu ya kutosha, kuna miti ya kutosha na hiyo ni taasisi ya umma. Ningeshauri viwanda vya kimkakati kama kile, laiti kama kingejengwa mahali kama Kilolo, Mufindi au Mafinga ambako kuna miti ya kutosha maana yake ni kwamba, hata shida ya madawati ingekuwa historia kwa sababu, kingeweza kufanya kazi nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba hizi taasisi za umma, taasisi kama VETA na magereza ambao wanataka kuwekeza kwenye viwanda waangalie mazingira, hasa hivi viwanda vya samani. Sasa kwenye huu Mpango iangaliwe, tunaposema viwanda vya kimkakati basi vijengwe kule ambako mazao hayo yanazalishwa badala ya kuweka mahali kwa sababu ambazo huenda haziwezi kuleta tija kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumzia ni kuhusu barabara, hasa TARURA, ambalo limezungumzwa na watu wengi. Naunga mkono wale wanaosema kitafutwe chanzo kingine, uundwe Mfuko mwingine wa peke yake na tuangalie kwenye sekta ya mawasiliano, ili tupate fungu la kutosha, tuweze kutatua changamoto ya barabara kwa sababu, baada ya hapo hiyo ndio itakayokuwa mwarobaini wa matatizo tuliyonayo, ili pia TANROADS iweze kubakia na hela za kutosha kwenye Mfuko wake ilionao sasa, kwa sababu, kama tukigawa kwa kiwango kikubwa tutaifilisi TANROADS na itashindwa kufanya kazi tutarudi hapa tena kulalamika. Kwa hiyo, Mfuko mwingine ni muhimu ili kwamba, tusiifilisi TANROADS na TARURA itafutiwe chanzo kingine ambacho kitasababisha pato la Mfuko wa TARURA kuwa stable.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, ningependa kuzungumzia suala zima la ajira kwa vijana na kuweka mazingira wezeshi na rafiki. Watu wengi sana wanamaliza form four wanapata division four na wengine wanapata division zero na hao wengi hatujawawekea utaratibu wowote. Tukiendelea hivi ina maana kwenye vijiji vyetu na kwenye maeneo yetu kuna vijana wengi ambao hawajawekewa mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza vyuo hivi vya ufundi vitakapojengwa, vyuo hivi vya kati, viangalie taaluma maalum kwenye haya maeneo. Ikiwa ni maeneo kama kule kwetu basi ufundi wa kutengeneza samani, ufundi wa aina mbalimbali, lakini pia kufundisha masuala mazima ya kilimo na aina mbalimbali za kilimo zinazolimwa kwenye maeneo husika, ili wale vijana wanaopata division four na wanaopata division zero tusiwaache bila kuweka mpango maalum kwamba, maendeleo yao ya maisha yao yatakuwaje kwa sababu ni wengi na hao watakuja kuwa watu ambao hawana kitu chochote wanachoweza kufanya. Hilo ni janga ambalo kama tusipoliangalia si jambo zuri kwa maendeleo ya Watanzania.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Kengele imegonga, ahsante sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante san ana naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii nami niweze kuchangia draft hii ya Mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza nianze kwa kuelekeza shukrani zangu kwa Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan kwa mambo mengi ambayo anaendelea kuyafanya na kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanaendelea kunufaika. Nitoe shukrani za pekee baada ya wananchi kutoa kilio cha bei za mahindi na kupelekwa kwake alitoa shilingi bilioni 50 kwa ajili ya ununuzi wa mahindi na fedha hizo kwa kweli zilifanya kazi kubwa tu ya kuhakikisha kwamba mahindi yananunuliwa na niliona mwenyewe kwa sababu hata Jimboni kwangu fedha hizo zilifika. Tunatoa shukrani nyingi sana kwa niaba ya wananchi wote ambao walinufaika na angalau bei ikaweza kuwa stable kidogo kutoka pale ilipokuwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye mambo machache ambayo nimeona ni vizuri nikitoa ushauri kwa Serikali wakati wa kuandaa mpango ambao tutakuja kuupitia utakapokuwa umekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza naomba niweke nyongeza kidogo kwenye ukurasa wa 68 wa Mpango unaohusu zao la chai, naomba niikumbushe Serikali kwamba wametaja Njombe, wametaja Lushoto, lakini Kilolo imesahaulika pale nafikiri ni makosa ya kiuchapishaji, naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili basi akafanya marekebisho kwamba pia nako kule kuna mashamba makubwa yana zaidi ya miaka 30 na nimeshasema hapa kwa muda mrefu hilo ninafikiri litakuwa ni kosa la kiuchapishaji kwa sababu Kilolo isingeweza kusahaulika kwa sababu hata Waziri wa Kilimo ameshatembelea tayari.

Kwa hiyo, nafahamu analijua, kwa hiyo utakaporudi mpango nitaiona kwa sababu ni kitu ambacho kinafahamika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sasa kilimo hasa kwenye mahitaji ya mbolea, nchi yetu inahitaji mbolea kiasi cha kama tani laki saba na hivi tunavyozungumza ukisoma mpango hata kwenye utekelezaji pale haukusema mbolea iliyokwisha ingia ni mbolea kiasi gani. Mpango pia hauoneshi mipango ya kuingiza hii mbolea kiasi gani zaidi ya kusema kuna kiwanda hapa Dodoma, kuna mwekezaji kutoka Burundi atajenga, kwa hiyo tunatarajia kitakapokamilika na hatujui hicho kiwanda kitakamilika lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa na watabiri wa hali ya hewa kwamba mwaka huu tutapata mvua za wastani au chini ya wastani, maana yake ni kwamba mikoa michache sana itakayopata mvua na hiyo ndiyo inayotegemea ilishe nchi yetu. Kwa hiyo upo uwezekano mkubwa wa kutokuwepo na chakula cha kutosha au kuwa na mabaa mawili baa la kwanza linalotokana na asili ambalo ni baa la kukosa mvua, lakini baa la pili ni baa ambalo tunalitengeneza wenyewe la kuto kutoa ruzuku kwenye mbolea na kusababisha mbolea hiyo iwe bei kubwa na kuwafanya wakulima wasinunue. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo wale wakulima wanasubiri mvua kidogo inayonyesha, kwa mfano baadhi ya Mikoa mvua zimeanza hawajapa hilo punguzo la hiyo mbolea wala ruzuku na wala Serikali mpaka sasa haijasema chochote kwa sababu ameshatoa maelekezo tunaamini kabla ya Bunge hili kuisha basi tutasikia. Pia kwenye mpango ili hii iwe endelevu ningependa kushauri kwenye mpango utakapokuja basi tujue ni mpango gani wa muda mrefu utakaofanya wakulima waweze kupata nafuu ya mbolea kama ilivyo kwenye nchi za jirani ambazo baadhi yake wengine wamezitaja walipokuwa wakitoa michango yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa kutoa ushauri ni kuhusu mikopo kwa vijana, akina mama na wenye ulemavu na hasa mifumo inayotumika. Ningependekeza kwenye mpango unapokuja sasa mwanzoni ilikuwa vikundi viwe vikubwa baadaye ikawa watu watano pendekezo langu ni kuwa, lengo la mikopo ile ni kuongeza ajira, mawazo ya kutengeneza mradi ili uweze kuleta ajira si lazima iwe watu watano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu mmoja anaweza akatengeneza mpango wa kukopesha watu na akaajiri zaidi ya watu ishirini wakati kikundi kinaweza kikawa cha watu watano na kikawa na mradi wa kufanya wao watano peke yao. Maana yake ni kwamba mpango uje na vigezo vinavyofanya hata kijana mmoja, hata mwanamke mmoja, hata mlemavu mmoja kukopa ili mradi anazalisha ajira nyingi kwa vijana, wanawake na watu wengine na hiyo itasaidia sana kwa sababu inaonekana wasiwasi ni uwezekano wa kulipa, kwa hiyo kuna dhamana zinazoweza kutengenezwa na nyingine zilishawahi kupendekezwa hata humu ndani, watu wapeleke vyeti ziwe dhamana wamemaliza degree zao au vitu vingine vyovyote vinavyoweza kuwa dhamana, au basi vijiji na maeneo watu wanaofahamiana vidhamini, lakini hii mikopo lengo ni kuzalisha ajira mtu mmoja apewe kusiwe na hii kusema wangapi ili mradi anazalisha ajira kwa watu wengi zaidi kwa sababu lengo ni kukuza uchumi ni kuweka mzunguko wa kutosha. Kwa hiyo, kigezo cha vikundi kinaelekea kupitwa na wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijikite pia kwenye kitu kingine cha miundombinu hasa vijijini kuhusu suala la barabara. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais ametoa fedha…

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Taarifa nafikiri inatoka Msekwa. Taarifa kutoka Msekwa, Mheshimiwa Jacqueline Msongozi nafikiri.

T A A R I F A

MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo. Nataka nimpe taarifa mchangiaji anayechangia sasa Mheshimiwa Nyamoga kwamba kuhusu suala la mikopo kwa vikundi itoshe tu kwamba Serikali inatoa pesa kwa ajili ya vikundi kwa maana ya asilimia 10 (4:4:2), lakini mikopo hii iwe yenye tija. Unakuta kikundi cha watu hamsini wanakopeshwa milioni mbili bado hiyo pesa haitaweza kuleta tija kwa watu hamsini shilingi milioni mbili. Kwa hiyo, ikiwezekana vikundi mbalimbali viwekewe pesa ya kutosha ili waweze kuanzisha hata viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Justin Nyamoga unaipokea taarifa hiyo.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea. Nijielekeze kwenye mpango wa TARURA, tumefurahi sana tumepewa wengine Bilioni 1.5, wengine Bilioni Moja kwa ajili ya barabara na kwa kweli fedha hizi zimesaidia sana tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu sasa kwa sababu ukiangalia tulivyojadili mwaka jana tulikuwa tunasema kwenye mfuko wa barabara iwekwe sheria zigawanywe ielekee... mpaka sasa TARURA ilianzishwa lakini chanzo chake cha mapato hakijawa kile ambacho ni mfuko kama ilivyo mifuko mingine, mfuko wa maji, mfuko wa barabara na mifuko mingine. Kwa hiyo tunagemea Mheshimiwa Rais akitoa kama hivi na tunamshukuru anaendelea kutoa na mwakani labda itafanyika hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ingekuwa kwenye huu mpango kama hizi fedha zipo na zinaendelea kuwepo basi ianzishwe programu kama ilivyo programu nyingine ambazo zimekuwa zikianzishwa na zinapewa fedha, labda iitwe Rural Road Maintenance Program na iwe na mipango kabisa ili tusiwe tunaenda kwamba leo kuna fedha tujue mpango huu labda ni wa miaka mitatu, miaka minne na tuta-cover barabara ngapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo TARURA ije wakati wakuja wana mpango, waje na mpango wa ukarabati wa barabara za vijijini unaoeleweka ambao utasababisha sasa fedha zinazopatikana zinapelekwa na zinaenda moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine ambacho ningependa kushauri kwenye mpango ikiwepo ni miradi ya kimkakati kwenye Halmashauri na nina uhakika kwa sababu hili suala ni la Wizara ya Fedha Mheshimiwa Waziri analifahamu. Vile vigezo vilivyopo vya kupewa miradi ya kimkakati tumekwisha kuvilalamikia sana kwamba vinatengeneza ubaguzi katika kunufaisha Halmashauri hasa zile zenye vipato vidogo na zile zenye hati chafu na hati zenye mashaka. Kwa hiyo, tulikuwa tumependekeza kwamba vigezo hivyo vipitiwe ili viweze kuwa rafiki kwa Halmashauri zote. Pendekezo langu ni kwamba mpango huo utakapokuja basi uwe unataja kwamba vile vigezo kwa sababu mara nyingine kwenye Kamati tulikuwa tumeambiwa unapitiwa basi tuambiwe kwamba vimepitiwa na vipo kwa namna gani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii na pia nakushukuru kwa muda uliotoa ili tuweze kujadili taarifa hizi tatu zilizowasilishwa na Kamati zetu. Awali ya yote, sishauri tuanze kufikiria adhabu ya kunyonga, kumnyonga mtu ni kumhamishia kwenye mamlaka nyingine ambayo hatuna udhibiti nayo na ni kumpelekea Mungu wahalifu ambao bado hatujashughulika nao. Hawa tushughulike nao kwanza hapa, itakapofika wakati wameshatubu basi ndipo waweze kunyongwa na kupelekwa huko. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kwenye mchango wangu nitajielekeza kwenye Kamati ya PIC kidogo, lakini pia na kwenye Kamati yangu ya USEMI. Kwanza nianze kusema kwamba, naipenda sana Wizara ya Kilimo na hii ni kwa sababu, jimbo langu ambalo wananchi waliniamini na kunileta linategemea sana kilimo. Mwaka huu wakati wa bajeti wote kwa pamoja tulipitisha kwa kauli moja kuongeza bajeti kwenye Wizara ya Kilimo na moja kati ya maeneo tuliyosema tuweke mkazo ni kwenye utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ili utafiti uweze kufanyika unahitaji vifaa. Ripoti ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali inasema TARI iliomba vifaa vyenye dola elfu 50 hatukuwa nayo. Bill & Melinda Gates wakatoa msaada, tena hata kabla hawajaachana hawa maana wameshaachana. Vifaa vile vikaletwa bandarini mwaka 2018, bandari wakavishikilia, vifaa vya utafiti vya virusi ambavyo vinaweza kuleta athari kwenye hii nchi na hicho kilimo chote kisiwe na maana, 2018, wakasema wanataka kodi. Msaada umeletwa mabilioni ya Melinda Gates, vifaa hivyo huenda pia vina vitendanishi ambavyo ni sumu vimebaki bandarini, hadi hivi tunavyoongea viko pale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumesikia juzijuzi kuna nchi bandari iliungua kutokana na kemikali. Sisi tunawekaje vitu hivi kwenye bandari yetu ambayo nina uhakika wanaovishikilia hawana utaalam huo na bado tunategemea hii nchi itaendelea kuwa salama ambapo tumeweka vitu ambavyo hata hatuvifahamu, lakini ambavyo vingekuwa vinatumika kwenye maabara sasa hivi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapata shida za magonjwa, virusi, kule kwangu mimi vitunguu kuna ugonjwa unaitwa kaukau hata hatuujui, maabara zetu vitendanishi viko bandarini toka 2018, kisa Wizara ya Kilimo imeomba msamaha. Ndio ile sasa jini likila kwingine linakula hata wakwake, Wizara ya Kilimo Serikali, imeomba msamaha kwa Wizara ya Fedha, msamaha 2018 hakuna, 2019 hakuna, 2020 hakuna, 2021 na leo hakuna, vifaa bado viko bandarini. Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali inasema vifaa hivi vinaweza kuharibika, vitolewe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo mengine sijui yanasubiri maazimio au hapahapa tu useme kabisa waweze kufanya maamuzi, mimi sijui, lakini kuna vitu vya hatari kama hivi ambavyo tusipovisemea tutakuwa hatuwatendei haki wananchi ambao wanasubiri kilimo ili kiweze kuwatia moyo. Hili ni jambo ambalo ni moja kati ya mambo unaweza ukayaona yaliyoko TRA kwa namna ambavyo tumekuwa tukitaja. Pia kuna taasisi hapa haupiti muda hatujazisema, tukija tunazisema, tukiondoka tunasema, nadhani huko nje wanasema, watasema watamaliza, halafu sisi tutaendelea na mtindo huo huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ufike wakati ieleweke kwamba, tunapokuja humu ndani tumetumwa na wananchi milioni 61 na wale wananchi hawawezi kuja huku kusema ndio wametutuma sisi ili tuwasemee, walipanga mstari tarehe 28 Oktoba, kutupigia kura ili sisi tuje tuwasemee mambo ambayo yanawaathiri wao, tukinyamaza tutakuwa hatuwatendei haki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiacha hilo la TARI ambalo linawaumiza wananchi kwa sababu, utafiti haufanyiki kwa sababu vitu viko bandarini kwa sababu Serikali inasubiri kodi kutoka kwenye Serikali yenyewe. Sasa naomba nizungumze kidogo kuhusu hao hao TRA ambapo wameng’ang’ania hivyo vifaa. Ukienda kwenye ripoti inasema kabisa, lita milioni 2.6 za mafuta ambayo yalikuwa yanasafirishwa kwenda nje hayakwenda nje, hiyo ni fedha yenye thamani ya bilioni 1.7, yalipotelea humu ndani. Ripoti inasema mafuta haya kwa kuwa hayakutoka maana yake yatakuwa yaliuzwa humu ndani na Serikali haikupata kodi. Sasa badala ya kushikilia vile vifaa kule si wangeenda wakakusanya hii fedha ya mafuta ya kodi ambayo inapotea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hii TRA iangaliwe. Wakati inaangaliwa ikumbukwe pia kwamba, hii ndio inayofanya ukusanyaji wa mapato makubwa zaidi ili iweze kuangaliwa vizuri, iangaliwe pia na watumishi wake idadi yake kwa sababu, ina upungufu wa watumishi 2,695 kwa mujibu wa Taarifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, ni mambo ya kuangalia ili tuweze kufanya vizuri na tuweze kutekeleza vizuri Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo ningependa kuzungumza ni mifumo ya taasisi tunazoziunda na dhamira yetu ya kuzifanya ziweze kuendelea. Nimesema pale awali mimi ni Mjumbe wa Kamati ya USEMI, hizi halmashauri zina chombo chake kinaitwa ALAT. Hiki chombo ambacho kinaitwa ALAT kinatarajiwa kuendeshwa kutokana na michango ya halmashauri, sasa kati ya mwaka 2015 na mwaka 2021, jumla ya bilioni
4.56 hazikupelekwa ALAT na kwa kutokupelekwa, hiyo ni asilimia 91 ya mapato ya hii ALAT, maana yake ni kwamba, haiwezi tena kujiendesha. Kwenye taarifa inasema kabisa kwamba, kuna hatari ya ALAT kushindwa kujiendesha kwa sababu haina mapato.

Mheshimiwa Spika, sasa ni vizuri tukatafakari tu kama haina haja ya kuwepo isiwepo, lakini kama kuna haja ya kuwepo, basi hizi halmashauri ambazo hazipeleki zipeleke ili iweze kujiendesha. Hii ndio ingeweza kuwajengea uwezo hawa halmashauri, hii ndio ingeweza kuwajengea uwezo Madiwani wetu ili waweze kufanya kazi vizuri, hawajachanga, hawajapeleka, ofisi iko pale na mimi huwa napita pale karibu kila siku, ni njia ya kule naona kibao ALAT, pale ipo, lakini hii ni ofisi ambayo imekusanya asilimia tisa tu ya mapato yake kwa miaka karibu nane, inawezaje kujiendesha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa kwenye maazimio yetu ni vizuri kuweka mkazo kwenye zile taasisi ambazo zilitarajia kuchangiwa na hazikuchangiwa na ambazo haziwezi tena kujiendesha ili ziweze kufanyiwa tathmini na kuona uhitaji wake na kuona namna zinavyoweza kujiendesha, kama haziwezi kujiendesha basi maamuzi yafanyike ili zisiwepo, kwa sababu mwisho wake ni kuanza kuzalisha madeni ambayo Serikali yetu itakuja kuanza kuhangaika kuyalipa hapo baadae.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie kidogo kuhusu hizi taasisi zetu. Mheshimiwa Sanga, aliyekaa alizungumza sana kuhusu GPSA, lakini tuzungumzie MSD ambayo pia imetajwa mara nyingi sana hapa. Huko nyuma nadhani kulikuwa na utaratibu wa taasisi kununua dawa MSD. Ikaonekana katika utaratibu huo MSD hailipi, Kwa hiyo ili kuweka utaratibu mzuri ikaamuliwa kwamba fedha ziende kwanza MSD halafu ndipo MSD ilete dawa. Sasa kibao kimegeuka, MSD inapewa hela na haitoi dawa. Kwa hiyo Bilioni 1.7 ambazo kila siku Waheshimiwa Wabunge tunalalamika, wananchi wanalalamika hakuna dawa, hizi fedha zililipwa MSD na MSD haikutoa dawa.

Mheshimiwa Spika, mwaka umekwisha, hizi fedha hazirudishwi kwenye Halmashauri na hazifanywi chochote. Kwa hiyo, kama mfumo huu ukiendelea maana yake ni kwamba MSD itakuwa inapokea hela zaidi ya kile ambacho huduma imetoa. Ushauri wangu ni kwamba iangaliwe mifumo ya ulipaji, huu wa GPSA na taasisi yoyote inayopata fedha kwanza, iwe GPSA, TEMESA, MSD au taasisi yoyote inayopokea hela kwanza, mfumo wake uangaliwe vinginevyo tuweke mtu kati, kuwe na taasisi ambayo hela ile inapelekwa, ukishatoa huduma unaenda unadai, siyo umeshapokea hela unakuwa sasa unaamua wewe unachotaka kukifanya, maana yake ni kwamba kunakuwa na ugumu kwa sababu tayari umeshalipwa, umeshapokea fedha. Sasa isipoangaliwa hii mifumo, hii hali itaendelea na hii ni hali ambayo inaweza ikawa changamoto katika utoaji wa huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wakati huohuo tuchunguze vizuri kwa nini dawa ambazo ni shida hazipatikani lakini kwenye taarifa inaonesha kuna dawa zenye thamani ya Shilingi Bilioni 7.3 zimeteketezwa. Inawezekana pia kuna changamoto kwenye mfumo wa uagizaji wa dawa, kwa hiyo dawa zinapofika kwa watumiaji zinakuwa zimebakiza muda mfupi na kwa hiyo zinatakiwa kuteketezwa. Sasa taasisi hizi ambazo zimetajwa mara nyingi humu zinatufanya tuone kuna haja ya kufanya maamuzi na maazimio yatakayoweza kukomesha jambo hili.

Mheshimiwa Spika, sisi umetuteua kwenye Kamati, tunakaa kule tunafanya maamuzi. Nakumbuka Kamati ya Bunge ya USEMI kwa mfano, Halmashauri zote zilikuja tukajadiliana nazo vizuri, wale ambao ni wa asilimia 10 tukawaambia. 2021 tuliwaambia asilimia 10 zote wapeleke kama ilivyopangwa, hawakupeleka! 2022 wamekuja wapo. Sasa tunawakuta ni walewale, Spika wewe umetutuma, tunawauliza tena walewale ambao tuliwatuma iliyopita na hawakufanya lakini wanarudi tena kwetu ni walewale.

Mheshimiwa Spika, hata kama ingekuwa wewe, yule mtu ulimwambia, hakufanya, anarudi unamwambia hakufanya! Hivi keshokutwa nakaa naye namwambia tena? Sasa ntamwambiaje ten ana mtu huyo hataki kutekeleza?

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo mimi naunga mkono hoja na ninaomba hatua kali zichukuliwe kwa wale wote ambao hawaitakii mema Serikali hii. Mungu awabariki sana, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote nichukuwe fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kuwepo hai hadi wakati huu, lakini jambo la pili niishukuru sana Wizara ikiongozwa na Waziri Mheshimiwa Bashungwa pamoja na Manaibu Waziri na watumishi wote katika wizara hiyo kwa ushirikiano ambao wanaendelea kunipa mimi pamoja na wananchi wa Kilolo katika kutekeleza majukumu yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Rais pia kwa jinsi ambavyo Kilolo imeanza na inaendelea kukumbukwa sasa kwa mambo mengi tofauti sana katika historia ya Jimbo la Kilolo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo madarasa ya sekondari 73 yamejengwe, shilingi milioni 800 Hospitali ya Wilaya karibu inakamilika kwa mara ya kwanza tangu uhuru tulikuwa na kituo kimoja cha afya, tunajenga vituo vya afya vinne kwa mpigo Ruaha Mbuyuni, Ilula, Nyarumbu pamoja na Ng’ulule vituo vinajengwa, lakini pia tunayo sekondari Kata ya Kimara haikuwa nayo inajengwa pamoja na mambo mengi nikiorodhesha nitamaliza muda wangu kwa kushukuru tu, lakini sasa naomba niende kwenye mambo mengine.Tunashukuru sana kwa ushirikiano ambao tunaendelea kuupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya kwanza nitakayoizungumzia inahusu mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo; zaidi ya asilimia 50 ya mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Kilolo inatengemea mazao ya misitu, mazao ya misitu tunayozungumza maana yake ni pamoja na nguzo, mbao na mazao mengine yanayofanana na hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nieleze ili Wizara ya TAMISEMI ijue athari zitakazotokana na maamuzi ya Wizara au idara nyingine za Serikali kuamua kununua nguzo nje ya nchi hii, tutakapoacha kununua nguzo kutoka kwenye Kiwanda cha New Forest kilichopo Wilaya ya Kilolo maana yake ni kwamba tujiandae kupunguza mapato ya Kilolo kutoka shilingi bilioni 4.5 sasa hizi kwenda shilingi bilioni mbili na point na kwa hiyo Serikali ijiandae kuleta fedha kuja kuweka hiyo nakisi hatutakuwa na hizo fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu kwa hiyo nataka Waziri anapoongea na Mawaziri wengine pamoja na Serikali inapozungumza ilijue hilo, athari za huo uamuzi ni nini kwenye mapato ya Serikali, ninaomba hili lieleweke vizuri ili nitakapokuja hapa kuomba fedha zaidi kutokana na kupunguza mapato baada ya hayo maamuzi ya kununua nguzo nje Serikali ikumbuke kwamba mimi nilisema na hii iwekwe kwenye rekodi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo langu la pili ni kuhusu miradi ya kimkakati; Mheshimiwa Waziri bahati nzuri ulikuwa Wizara ya Viwanda na Biashara na ulitembelea Kilolo na bahati nzuri ulitembelea mashamba ya chai, nataka nikuambie mradi wa kimkakati uliletwa mwaka 2018 kwa ajili ya ununuzi wa mitambo kujenga kiwanda kile cha chai hata jibu hadi leo halijawaji kupatikana kwamba ni mbovu, una nini, hatujapata jibu na kiwanda hakijajengwa na bahati nzuri na Waziri wa Kilimo yuko hapa anajua tunavyoangaika kutafuta fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, mmejenga masoko sawa, mmejenga stand huko sawa mngetuambia basi sisi Kilolo tumekosea nini kwenye kuandika ili tuweze kupewa fedha tuweze kujenga kile kiwanda cha chai ambacho kinaajiri watu 2,000 na sisi kwetu watu 2,000 ni wengi, ambacho kitaongeza uzalishaji kwenye chai na tutaongeza mapato ya Halmashauri kwa sababu yale mashamba yanamilikiwa kwa asilimia 40 na Halmashauri, kwa asilimia 10 na Msajili wa Hazina ambayo ni Serikali tena hiyo Hazina inayotoa hela hayo mashamba yanamilikiwa kwa asilimia 50 na wananchi kule hayamilikiwa na taasisi binafsi, inashindikanaje kutoa fedha kwa ajili ya ule mradi wa kimkakati pale?

Mheshimiwa Naibu Spika, ninalo lile andiko kama limepotea au liko mahali niko tayari kukuletea twende mguu kwa mguu Hazina tupate zile fedha kile kiwanda kipate kujengwa na mitambo inunuliwe na zile hela sio nyingi ni kama tu shilingi bilioni tatu ambazo kule mmetoa shilingi bilioni 60 majengo makubwa tunashindwaje kutoa fedha kidogo hivi kwa ajili ya kiwanda cha chai kilichokaa miaka 30 hakijengwi na hela zipo kila siku tusomee miradi ya mkakati ya mijini na sisi tunataka hizo fedha kwa ajili ya mradi wa kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya jambo hili naomba pia nizungumzie kuhusu vifaatiba; ninashukuru sana kwamba umejengwa vituo vya afya vizuri pale Ruaha Mbuyuni mmetupa na hata shilingi milioni 300 juzi tumalizie maana kile kilianza kujenga mwaka wa fedha uliopita na pia pale Ilula tunacho na ninyi mnajua haya ni maeneo ya barabara kuu, sasa hivi karibuni kulitokea ajali pale Ruaha Mbuyuni watu walipelekwa pale nadhani ni kama watu tisa au kumi ambao walihitaji huduma kwanza, madaktari hakuna, lakini vifaatiba havipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maeneo kama haya tumeambiwa kuna ajira zinakuja maeneo ya barabarani, maeneo yenye Vituo vya Afya ambavyo vinahitaji attention kubwa kwanza madaktari wapelekwe, lakini pili tutafute uharaka wa kupeleka vifaatiba kwa sababu pale sikutakiwa peke yangu nisimame, Wabunge wote humu mnapita Ilula, Wabunge wengi humu mnapita Ruaha Mbuyuni mnapoenda kwenye sehemu zenu huko, hili ni suala la sisi wote na wananchi wote wanaopita mle kwa sababu hatuwezi kujua ya kesho, ninaomba sana vifaatiba kwenye hivi vituo vya afya viwili ambavyo vimekamilika, ninawashukuru sana vifaatiba vipewe kipaumbele kwa sababu ya unyeti na umuhimu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna jambo moja ambalo ningependa kulizungumzia nalo ni suala zima la TARURA pamoja na fedha na jinsi zinavyotolewa, mambo mawili; jambo la kwanza ni suala zima la magari ambalo limeshazungumzwa na vifaa, tulipokuwa kwenye Kamati mimi ni mwamakamati wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, tulipokuwa kwenye kamati tuliona kwamba kweli fedha za magari zimetolewa, lakini mamlaka zinazonunua hazijanunua zaidi ya magari 100 na fedha zimeshalipwa, haya magari yangeweza kugawa kwenye hizi Halmashauri yangetosha, kupunguza angalau hiyo kero.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuiombe Serikali kwa sababu ni hiyohiyo tujue kikwazo kinachozuia magari haya kununuliwa na kugawiwa kwa hawa hiyo mamlaka ingekuwa ni taasisi binafsi imepewa fedha za magari zaidi ya 100 hainunui mwaka mzima, hicho ni kiashiria kinaweza kupeleka hadi kwenye karibu na uhujumu, sasa ni Serikali hatuwezi kuita hivyo. tunafanyaje kuhusu watendaji au mahali popote panapokwamisha ununuaji wa haya magari? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini jambo la pili TARURA ina sema kwamba wanasajili barabara, sasa barabara inayosajiliwa ni kwamba imetengenezwa yako maeneo kama kule kwangu kwa mfano pale kutoka Idete ili ushuke kule Mngeta ni pori, pana mchoro wa barabara, lakini ni msitu, kila tukienda pale wanasema tengenezeni ili tusajili, atengeneze nani na ile ni hela nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu ni lazima itobolewe ile barabara kama ingelikuwa ni ndogo kwa hela ndogo lakini barabara kubwa kama ile lazima itengewe fedha ili itoboke na ile ni barabara muhimu kiuchumi, ndio tungeweza kusafirisha mbao kwa treni kwenda Dar es Salaam, lakini hatuwezi kuitoboa kwa mikono, walijaribu pale walienda wananchi walishindwa ni sehemu ambayo ni lazima Serikali iwekeze. Ninaomba TARURA kwa dharula itenge fedha kwa ajili ya kutoboa barabara ile ili iweze kufanikiwa na kufanya kazi. Nakuomba sana kupitia kwako namuomba sana Waziri aingalie barabara kama hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na barabara nyingine ambazo ni muhimu kiuchumi nataka kuwakumbusha Waheshimiwa Wabunge mkila njegele, viazi na hizo mbogamboga nyingine zote kwa asilimia kubwa zinatoka Kilolo.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara kama ya kutoka Kitoo kwenda Masisiwe, barabara kama ya kutoka Ihimbo kupitia Itimbo kuja kutokea Kitelewasi ambako ndo mahindi mengi mnakula haya ya njiani, barabara ya kutoka Nyanza kwenda Mtandika vitunguu karibu vyote vinatoka huko hizi barabara zinahitaji ile milioni mia tano tu na ndio maana wakati ule nikakuambia mimi nikipata shilingi bilioni 1.5 inapunguza sana hizi kero. Lakini si kwa ajili yangu tu ni kwa ajili ya Watanzania wote wanaoatarajia mazao kutoka kule lakini pia kwa ajili ya kuongeza mapato ambayo yanaweza kutusaidia.(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote na mimi nichukue fursa hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi leo tuweze kuchangia hoja iliyoko mezani. Nianze kwa kutoa shukrani zangu kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa jinsi ambavyo amei-support vizuri sekta ya elimu hususani katika jimbo langu la Kilolo lakini na nchi nzima kwa ujumla. Tunayo mengi ya kusema lakini tushukuru sana kwanza kwa ahadi yake ya kujenga vyuo vya ufundi VETA ambavyo pia Wilaya ya Kilolo ni wanufaika na ujenzi unaendelea hivi tunavyozungumza; tunaona kazi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nishukuru kwa ujenzi wa shule za wasichana za mikoa ambapo kwa Mkoa wa Iringa itajengwa katika Wilaya ya Kilolo. Ninafahamu kwamba maandalizi yanaendelea na sisi tunaisubiri kwa hamu, tumejiandaa tumejipanga na eneo lipo tayari. Ni kazi tu ya kuanza ujenzi ndiyo inayosubiriwa. Kwa hiyo tunashukuru sana kwa kazi zinazofanywa na Mheshimiwa Rais na sisi tuko tayari kushirikiana naye na kuendelea kumuunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nipongeze juhudi zinazofanywa na wizara katika kuboresha mitaala ambayo imekuwa ni kilio chetu muda mrefu humu ndani. Mimi ninaamini majadiliano yanayoendelea yatatupa mtaala bora ambao utaendana na mazingira na hali ilivyo kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninao ushauri katika masuala machache ambayo yanaenda kwenye Sera ya Elimu na taratibu mbalimbali, na nianze kwanza na suala la udhibiti ubora. Lakini nizungumzie kidogo kipengele cha mitihani na nizungumze jinsi wasimamizi wa mitihani wanavyopatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, walimu wanaofundisha shule mbalimbali za sekondari huchukulia kwamba ule usimamiziwa mitihani ni fursa kwao kwa namna mbalimbali kama vile kukua na kujifunza, kusimamia pamoja na kusahihisha. Kukua na kujifunza kuelewa zaidi lakini pia ni fursa kwao kwa sababu ina kipato pia zaidi. Sasa, namna wanavyopatikana hakuna uwazi wa kutosha wa kuwafanya wale ambao hawakuchaguliwa waridhike kwamba na wao hawakuchaguliwa kihalali.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependekeza kwamba kuwe na utaratibu mzuri wa uchaguzi wa walimu wanaosimamia mitihani na vigezo. Yaani kuwe na mwongozo mzuri unaosema vigezo vya walimu wanaosimamia mitihani namna wanavyopatikana, wale wanaosahihisha mitihani na namna wanavyopatikana, ili kuondoa malalamiko au kuondoa mtu mmoja kuhodhi maamuzi ambayo inawezekana inaweza kupelekea mianya ya rushwa kwa walimu wetu ambao pia vipato vyao si vikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo ni la kwanza, ningependekeza hata tunavyotengeneza sera pia iangalie hicho kipengele, kwamba ni namna gani usimamizi na usahihishaji wa mitihani unafanyika na hao wanaofanya hiyo kazi wanapatikanaje. Ikiwa wazi kwa namna yoyote ile inapunguza malalamiko kwa hiyo linakuwa ni jambo ambalo linauwazi wa kutosha, hilo ni jambo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo kisera halijakaa vizuri; wote tunajua kwamba watoto katika shule zote, chekechea, msingi, na sekondari, sasa hivi hizi shule nyingi ni shule za kutwa, liko jambo la chakula cha mchana, sasa jambo la chakula cha mchana limetiwa nguvu sana na umuhimu wa lishe bora kwa watoto wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili ni jambo jema na wazazi wamelipokea vizuri. Katika mazingira ya elimu bila malipo wanafunzi wengi wanachangia. Lakini nataka nikupe scenario moja, unakuta kwenye kata kuna shule mzazi anatakiwa kuleta mahindi debe moja kila mwezi lakini kuna shule mzazi anatakiwa kuleta debe tatu kila mwezi na mwingine anatakiwa kuleta kilo tano kila mwezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa kawaida sisi wote tuna utaalamu wa kutosha wa kujua ratio za chakula kwa sababu tunazo shule za bweni tunajua Watoto wanatakiwa kula nini mchana. Utaratibu ambao ungeweza kuwa mzuri ni mwongozo wa uchangiaji wa chakula kwenye hizi shule ili kusiwe na mtu anaamua tu. Ndiyo maana wazazi wakati mwingine wanakuwa wagumu kuchangia kwa sababu hakuna kigezo kinachotumika kujua ratio ya mwanafunzi ya chakula lakini yule anayeamua mengi anaweza akawa na nia ovu, inatoa fursa au mwanya kwa mtu ambaye yeye ana mipango yake ya kuchangisha chakula zaidi kwa jambo la kwake yeye aweze kufanya hivyo kama Wizara haikutoa muongozo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba Wizara ya Elimu fanyeni utafiti njooni na ratio ya chakula mtoto anachotakiwa kula ili mzazi aambiwe kwa mujibu wa taratibu unatakiwa kuchangia hiki ili mtoto wako ala chakula cha mchana, na hiyo itapunguza kabisa malalamiko yale yanayojitokeza. Na itapunguza, wakati mwingine unakuta wamekusanya mahindi yamebaki shuleni kwa sababu walichangisha zaidi au wakati mwingine ni majaribu sasa kwa walimu wale kupata majaribu sasa ya kuuza au kufanya jambo lingine ambayo inapelekea mwakani uchangishaji unakuwa mgumu. Suala hili ni la miongozo. Kwa hiyo mshirikiane na TAMISEMI kutoa muongozo mzuri ili hili nalo liweze kwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni kuhusu mikopo ya vyuo vikuu. Kuna changamoto ndogo ambapo mtu ameomba mkopo hakupata. Kimsingi huwa mtoa tu majina hamuwezi kumwambia kwa nini hukupata, na kwa sababu hajui anakata rufaa akikata rufaa majina yanatoka tena hayasemi tena kwa nini rufaa yake haikukubaliwa; mwakani anakata tena rufaa hivyohivyo mpaka akiendelea kujaribisha mpaka atakapopata. Nafikiri mifumo ya rufaa huwa inamrejesho. Kwa sababu ni vibaya kuendelea kumtumainisha huyu mtu kwamba akikata rufaa mwakani atapata. Kwa hiyo kama bodi imeona kuwa huyu mtu hakopesheki imjulishe kwamba wewe hautakopeshwa mpaka utakapomaliza miaka yako mitatu ili asiendelee kupata shida ya kukata rufaa kukata rufaa wakati kiukweli bodi imesharidhika kwamba huyu mtu hakopesheki na impe majibu kwamba kwa nini hakopesheki.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili tumelizungumza muda mrefu hapa bungeni; kwa sababu wakati mwingine unakuta huyu ni mtoto kweli wa maskini labda au alisoma shule za kanisa na kwa hiyo pengine au shule hizi za binafsi kwa kulipiwa na mfadhiri na vigezo vingine vingi. Sasa kadiri ambavyo anazidi kukata rufaa anategemea; ni kama bahati nasibu. Mimi nisingependa bodi ya mikopo ifanye kukata rufaa kama bahati nasibu. Kwamba sijui nitapata au sijui sitapata tena; anakata rufaa wakati mwingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwe na mfumo wa taarifa, yaani wa mrejeshi. Kwamba sababu ambazo zimekufanya usikate ni hizi na kwa hiyo kama hazitarekebishika hautapata, au wewe usiombe tena kwa sababu umekataliwa, au wanaoruhusiwa kukata rufaa watolewe orodha kwamba ninyi mnaweza kukata rufaa. Kwa hiyo hao watu wataona pale kwenye orodha; kwamba hawa ndio mnaoweza kukata rufaa na hawa hawawezi kukata rufaa ili shughuli ziendelee na wale ambao hawastahili kukata rufaa wa sikate rufaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine la mwisho ambalo ningependa kuzungumza ni namna elimu inavyosimamiwa, na hasa kwenye Vyuo Vikuu. Tunavyo sasa vyuo vikuu ambavyo vinasimamiwa na Wizara moja kwa moja lakini kuna vyuo mbalimbali vinavyosimamiwa na Wizara nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninafikiri hili ni suala la Elimu kwa sababu watoto wote wanaosoma wanatarajia kuingia kwenye soko la ajira kwenye sekta zote. Yaani kama ni kwenye Serikali za mitaa wanatakiwa kuingia kwenye sekta zote. Kama ni kwenye sekta ya fedha wataingia kwenye sekta zote. Kama ni kwenye sekta ya michezo wataingia kwenye sekta zote kama kila Wizara itaanzisha chuo kwa ajili ya watu wa taaluma yake vile vyuo vikuu vingine vinakosa relevance.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ningefikiria kwamba kuwe na mfumo tu mmoja wa vyuo vikuu vyote na viwe vinasimamiwa na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na kwa hiyo watoto wanapomaliza wote wanakwenda kwenye utaratibu wa kutafuta ajira, kunaweza kukawa na vyuo vyenye msisitizo wa jambo fulani. Kwa hiyo kunaweza kukawa na vyuo vya madaktari ambavyo havisimamiwi na Wizara ya Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kunaweza kukawa na vyuo vya watumishi wa Serikali za mitaa ambazo hazisimamiwi na TAMISEMI, au vyuo vya michezo ambavyo havisimamiwi na Wizara ya Utamaduni Sanaa na Michezo kwa sababu mwisho wote wanomaliza wanaingia kwenye soko la ajira moja na kwa hiyo hakuna sababu ya kwamba vyuo hivi visimamiwe na watu wengine. Lakini pia Serikali ni moja; kwa hiyo sualala uratibu wa elimu likiratibiwa na sehemu moja, hasa kwenye hii mitaala tunayoendelea litakuwa jambo zuri kwa sababu uratibu ule utafanyika kwa uzuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa niwakumbushe tu kwamba kwenye upungufu wa walimu kwa kweli baadhi ya wilaya zilizoko pembezoni zina shida sana, hasa kwa mfano Wilaya ya Kilolo, kuna maeneo kwa kweli ni changamoto, tunaona walimu wawili watatu. Kwa hiyo changamoto ya walimu pia kwa kushirikiana na TAMISEMI inapofika wakati wa kuitatua basi tuangalie pia maeneo ambayo yana changamoto kubwa ili yaweze kuapta kipaumbele katika kupangiwa walimu zaidi na ili hiyo changamoto iweze kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja na ninakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii kushukuru kwa nafasi hii niliyoipata. Nichukue fursa hii pia kukishukuru Chama cha Mapinduzi kwa kuendelea kusimamia Ilani ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwanza kwa kuleta shukrani kutoka kwa wananchi wa Jimbo la Kilolo. Wengi wameshukuru uongozi wa Rais wetu Hayati Dkt. John Joseph Pombe Magufuli kwa mambo makubwa aliyoyafanya. Wananchi wa Kilolo wanamshukuru na watamkumbuka kupitia mambo mbalimbali ambayo waliyapata katika kipindi cha awamu iliyopita na wamenituma nishukuru kwa mambo haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, wanashukuru kwamba Mji wa Ilula ambao haukuwa na maji kwa miaka mingi sasa una maji ya kutosha na ni kupitia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Wanashukuru sana Wizara ya Maji kwa kuwapatia maji watu wa Mji wa Ilula. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, watu wa Kilolo wanashukuru kwa mara ya kwanza kwenye vijiji wamepata barabara ya lami kilomita 18 kutoka Kidabaga - Boma la Ng’ombe. Mheshimiwa Naibu Waziri wa TAMISEMI ametembelea ameona barabara ile inaendelea kujengwa. Wanashukuru sana na watamkumbuka Hayati Dkt. John Joseph Magufuli kwa jambo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wanashukuru kwa sababu wamejengewa hospitali ya wilaya. Wanaishukuru sana Wizara ya Afya na Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwamba kwa mara ya kwanza Wilaya ya Kilolo ina hospitali nzuri ya mfano ambayo itatibu watu wengi na watu wale wataondokana na kero waliyokuwa nayo ya maradhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kati ya mengi yaliyofanyika ambayo wananchi wa Kilolo hawatamsahau Dkt. John Joseph Pombe Magufuli katika uongozi wake niliona nitaje hayo machache. Kwa niaba ya wananchi ambao wamenituma, hayo yamefanyika na yanaonekana na ndiyo ambayo ni kielelezo cha utendaji mzuri wa Serikali ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi hao pia wamenituma nikumbushe mambo machache kwa Serikali hii sikivu. Jambo la kwanza wameniomba nikumbushe kwamba ile barabara ambayo ni ahadi ya kutoka Iringa Mjini kwenda Kilolo hadi Idete bado barabara ile inaendelea kujengwa lakini haijakamilika. Wanaamini Serikali hii sikivu itatekeleza hilo kwa sababu imo kwenye ahadi na kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wananchi hawa wa Kilolo wanakumbusha kwamba mara kwa mara viongozi waliotembelea pale Kilolo akiwepo Waziri wa TAMISEMI, Waziri Mkuu Mstaafu Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda kwa kuona ukubwa wa Halmashauri ya Kilolo waliahidi kuigawa Halmashauri ile na kuwa Halmashauri mbili na pia kuelekea kugawa lile eneo kuwa Majimbo. Jambo hili lipo TAMISEMI hasa la halmashauri na wananchi wale wa Kilolo wanaomba kupata majibu ni lini sasa halmashauri ile itagawanywa ili kupata halmashauri mbili ili kurahisisha utekelezaji wa mambo mbalimbali hasa kuleta karibu huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wanakumbusha kwamba kuna ahadi ya Mheshimiwa Waziri Mkuu alipofanya ziara ambayo ni ya kituo cha afya pale katika Mji wa Ilula. Nayo pia wanaikumbusha kwamba Serikali iangalie na kwa kuwa hii ni bajeti ya Waziri Mkuu basi wanaomba kukumbusha hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa ujumla wake niendelee kukumbusha ajira kwa vijana hasa walioko katika shule za sekondari ambao wanajitolea; walimu wa kujitolea kwenye shule mbalimbali wa masomo ya sayansi. Wako wengi hata katika Jimbo la Kilolo lakini na katika maeneo mbalimbali, hilo pia tunakumbusha kwamba liendelee kuangaliwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye….

NAIBU SPIKA: Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukruu sana, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa maoni yangu kwa maandishi kama ifuatavyo; kwanza naipongeza sana Serikali hasa Wizara ya Kilimo kwa ushirikiano mkubwa ambao Wilaya ya Kilolo tulipata wakati wa kukarabati scheme ya Ruaha Mbuyuni baada ya mkondo wa maji kuhama kutoka katika scheme hiyo. Kwa namna ya pekee napongeza moyo wa kujituma wa watumishii wa Wizara waliotumwa kufanya kazi ile kwa umahiri na weledi wao.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizi, napenda kutoa maoni yafuatayo kwa Wizara; nakupongeza wewe Waziri na Naibu Waziri kwa ushirikiano pamoja na Katibu Mkuu na Mkurugenzi wa Umwagiliaji.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ni mpango wa Serikali kugawa miche bure kwa mazao ya kimkakati kama ilivyo kwa kahawa na michikichi nashauri Wizara ianze mara moja kuotesha na kugawa miche ya parachichi bure katika Wilaya ya Kilolo ambayo kilimo hicho kinakuwa kwa kasi kubwa na ni mkombozi katika mazao ya biashara. Tayari nimefanya maongezi na Naibu Waziri wa Kilimo na Mkurugenzi wa TARI kuhusu suala hili, hivyo naomba msukumo wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, nafahamu Wizara inazo taarifa kuhusu shamba la chai la Kidabaga ambalo lilikuwa linamilikiwa na TTB na ambalo ni miaka 30 sasa tangu limetelekezwa. Lakini pia katika eneo la Kidabaga na kata za jirani wapo wakulima waliolima chai yao na wanaendelea kusubiri kiwanda cha chai kwa miaka hiyo yote. Hivi sasa kuna tishio la wananchi kung’oa chai hiyo na kupanda mazao mengine baada ya uvumilivu wa miaka mingi bila mafanikio.

Naiomba Wizara kwa kushirikiana na Wizara ya Uwekezaji na Wizara ya Viwanda na Biashara mlete majibu ya ufumbuzi wa kiwanda cha chai cha Kidabaga. Nitashukuru kama kwenye hitimisho lako utakuja na majibu ya suala hili.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Tume ya Umwagiliaji wapo wafanyakazi wa tume wamewekwa kwenye ngazi ya mkoa. Kwa bahati mbaya watumishi wale hawana bajeti na sina uhakika kama wana maelekezo ya kutosha kuhusu kazi zao na uhusiano na Halmashauri zetu. Naomba jambo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, zao la pareto ni kati ya mazao ambayo sasa yanapanda katika soko la dunia, wapo wakulima katika Wilaya ya Kilolo naomba kusiwe na urasimu katika upatikanaji wa vibali vya wanunuzi kwenye zao hili.

Mheshimiwa Spika, kuna magonjwa ya mazao hasa nyanya yamejitokeza ambayo hayakubali dawa zilizopo, naomba timu ya wataalamu itumwe kwa ajili ya uchunguzi.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa uhai na afya ili niweze kushiriki kuchangia Bajeti kuu. Jambo la kwanza, nichukue fursa hii kwa niaba ya wananchi wa Kilolo kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi nzuri sana anayoifanya. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu na ofisi yake kwa kuwasilisha bajeti nzuri yenye mwelekeo na dira nzuri kwa ajili ya maendeleo ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza bajeti hii kwa sababu za msingi kabisa. Bajeti ya mwaka jana 2022 ilikuwa na Shilingi bilioni tatu kwa ajili ya shule za wasichana za mikoa inayojengwa Kilolo. Nina sababu ya kupongeza. Pia kuna kilometa 33 za barabara kutoka Ipogoro mpaka Kilolo, nina sababu ya kupongeza. Vile vile tumesema juzi tu kuhusu bypass ya Mlima Kitonga, kilometa 10, usanifu tumeshauona kwenye bajeti ili angalau watu wasikwame pale, tuna sababu ya kupongeza. Pia hii bajeti ina miradi mingi sana kwa ajili ya Kilolo; miradi ya VETA, miradi ya maji, ina mabwawa na mambo mengi mbalimbali, lakini na ruzuku ya mbolea na Kilolo ina maeneo mengi ya wakulima, nina sababu ya kupongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, nami naamini kwamba kwa mwenendo huu nchi yetu inaenda kupata sura mpya ya maendeleo katika uongozi wake. Nami namwombea maisha marefu, Mwenyezi Mungu ambariki ili aendelee kuwatumikia Watanzania katika kipindi ambacho Mwenyezi Mungu amempa nafasi hiyo kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nije kwenye hoja chache ambazo ningependa kuchangia kwenye hii Bajeti Kuu. Jambo la kwanza, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kupiga marufuku maduka yasifungwe kwa sababu yoyote ile. Naomba nimwongezee kitu kimoja, naomba atakaposimama pia aagize magari yasikamatwe yanapokuwa yamebeba mizigo ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, iko hivi, mtu anatoka mjini, amenunua vitu vyake, amepakia kwenye gari, ile gari siyo yake, lakini aliyenunua vile vitu hajadai risiti, na yule mtu anaenda anafika, gari inakamatwa. Ile gari ikikamatwa inapelekwa yard. Ikipelekwa yard, kama ni Ijumaa ni hadi Jumatatu, na huyu mtu ni mfanyabiashara, na gari ile siyo ya yule aliyefanya kosa na aliyefanya kosa anajulikana. Kwa hiyo, huyu mwenye gari anapata hasara kubwa ya kutoendelea na biashara yake kwa sababu ya yule ambaye hakudai risiti. Kwa sababu anayenunua, haendi na mwenye gari dukani, wala hajashiriki hilo kosa la kutokudai risiti. Kwa hiyo, napendekeza kutokufunga maduka kuambatane pia na kutokukamata magari yale yaliobeba mali ili yale magari yaendelee na shughuli zake. Hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili linalohusiana na mambo yaliowekwa kwenye bajeti hii kuhusu kodi ni suala la faini ile ya kutokudai risiti ile ya Shilingi milioni nne hadi Shilingi milioni tatu. Ni ukweli usiopingika kwamba ile ilikuwa inatengeneza kichaka cha rushwa, kwa sababu kama mimi nina mzigo wa Shilingi 300,000/= na sikudai risiti, hata gari ikipelekwa yard siwezi kupata hiyo Shilingi milioni tatu wala milioni nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona pale kuna pendekezo la punguzo, lakini Mheshimiwa Waziri naomba wasaidizi wako waangalie lile punguzo vizuri ili liendane na bei ya mzigo huu ambayo sikudai risiti. Huwezi kumdai mtu ambaye hakudai risiti ya shilingi 50,000, umwambie alipe shilingi milioni tatu hadi shilingi milioni nne, kwa sababu hana na kwa hiyo, mara nyingi unafungua milango ya majadiliano tu ya rushwa ili aweze kuondoka na huo mzigo wake. Kwa hiyo, hilo pia ningeomba niwasilishe kwa namna hiyo kwamba pia liendelee kuangaliwa ili lisiweze kuleta changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningependekeza jambo moja kwenye mambo ya kodi, katika kipindi cha hivi karibuni, tulimshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwani aliwaagiza TRA kuangalia zile kodi ambazo ni za muda mrefu zisiweze kulipwa, lakini kuna tafsiri nyingi sana kwenye hizo kodi za muda mrefu. Pale Iringa kuna mlipakodi mkubwa tu alikuwa anadaiwa kodi ya VAT lakini alipoenda akasema hizi zote zimeshasamehewa. Kwa sababu muda mrefu wenyewe yeye alitafsiri labda ni wiki moja, wiki mbili, wiki tatu, mwezi au mwaka. Kwa hiyo, napendekeza ofisi yenu inayo wajibu wa kutoa tafsiri ya huo muda mrefu na aina ya kodi ambazo zimepata huo msamaha ili kusitokee watu wa TRA kuwaonea wale ambao hawakupaswa kulipa wamesamehewa, lakini pia wale wanaotakiwa kulipa walipe bila kutumia hiyo kama kivuli cha kujitetea kutokulipa kodi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda mliangalie ili mlipe tafsiri ya hiyo kauli, pia mpeleke kwa maandishi maelezo TRA ili wale vijana wanaosimamia hizo wasijiamulie wenyewe kwamba hii ndiyo iliyofutwa, hii haikufutwa. Kwa hiyo, hilo nafikiri ni vizuri mkaliwekea mkazo na mkaangalia katika utaratibu huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la kikodi, napenda kuzungumzia zaidi hii kwa sababu tunachangia bajeti na ni mapato na matumizi, ni kuhusu kuweka utaratibu mzuri kwenye mazao ya kilimo ambayo hayawezi kuwa na risiti za EFD. Kila kitu kimewekwa EFD, gari zinazobeba mchanga EFD na ukweli hamjasambaza hizo EFD kwamba magari yanayosomba michanga huko hayana EFD lakini na wao wanadaiwa EFD. Sisi tunaotoka kwenye maeneo ya kilimo tunapata shida sana kwa wakulima ambao wanataka kuuza mazao yao, kila siku ni lazima wachukue barua ya Mtendaji wa Kijiji, wapite TRA wachukue barua; anakuwa na barua karibu tano, kwa nini? Kwa sababu tu ajieleze kwamba yale mazao ni ya kwake ameyavuna shambani anayapeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, huo usumbufu wa aina hiyo, utengenezeeni utaratibu ambao hausababishi hiyo kero. Pamoja na hizo barua zote, ukifika hapo Migori bado utakamatwa na hadi bei ya rushwa inajulikana, kwamba ukifika pale, ukitoa shilingi 200,000 ndiyo unapita. Kwa hiyo, sasa hii inakuwa pia ni mwanya wa rushwa ambao siyo mzuri. Kama kuna changamoto yoyote, kama ni mbao, kama ni njegere, kama ni viazi tunapopita pale ieleweke, nimetokanavyo shambani. Hata kama hukutokanavyo shambani, ukinunua kwa wakulima, umekusanya, hauna EFD na hawajapewa na huwezi ukawagawia wakulima wote EFD. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, uwekwe utaratibu mzuri ili iwe ni routine kwamba upo utaratibu, badala ya sasa hivi ambapo ni uamuzi wa unayemkuta getini kwamba inakuaje? Hiyo inawasumbua wakulima wetu sana, kwa sababu kila siku lazima watakupigia simu, “eeh, nipo hapa getini, leo wamenisumbua.” Unaanza tena kupiga simu kwa huyo mtu ili awaruhusu. Sasa hiyo inakuwa ni kero na nafikiri ni vizuri mkiiwekea mkazo ili iweze kutatuliwa na wakulima waweze kusafirisha mazao yao bila shida yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mimi sisemi wasilipe kodi, kama kuna kodi inatakiwa kulipwa, wekeni utaratibu mzuri wajue. Ile rushwa ambayo inatolewa pale, ile Shilingi laki mbili mbili, basi iwekeni angalau basi iwe ni Shilingi laki moja, ipungue nusu, iingie Serikalini badala ya kila siku kuacha Shilingi laki mbili pale kwa mtu. Nafikiri ile ingeweza kuwa ni suluhisho kubwa zaidi kuliko kujua kabisa kwamba nikienda pale ni lazima niwe na shilingi 200,000 na inaenda kwenye mfuko wa mtu. Hilo napenda liwe hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mawili ya mwisho, kwenye bajeti zijazo, hebu tuangalie, hiki chanzo cha hewa ya ukaa kimekaaje? Kwa sababu tunaona wawekezaji binafsi, mtu ana hekta 5,000 tu pale Kilolo anapanda miti, analipa watu hela nyingi tu anakuwanazo, huyo ni mwekezaji binafsi. Sisi Kilolo tuna hekta 52,000 za miti ya asili, hatulipwi hata buku na mtu yeyote. Sasa najiuliza, huyu amekuja amepanda hekta 5,000, analipwa hela, analipa watu 200 wafanyakazi kwenye ardhi yetu, sisi wenye hekta 52,000 hata buku hakuna. Kwa utaratibu upi? Hiyo bado nafikiri Serikali pengine iunde kikosi kazi kifanyie kazi. Hizo nazo ni hela atakuwa anapata, na Mheshimiwa Waziri utapata hela nyingi zaidi, pengine hata kodi nyingine zitapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. JUSTUN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, kuna haya mashindano ambayo yanaandaliwa na Waheshimiwa Wabunge yaani mfano Mchengerwa Cup, Bashungwa Cup na mengine, hivi haiwezekani kutenga bajeti kidogo na kuchangia kama ambavyo Mfuko wa Jimbo upo? Jambo hili litakuza michezo majimboni na kuwapunguzia Wabunge mzigo mkubwa wa kununua mipira na jezi. Tunaweza kutumia fedha ya Mfuko wa Michezo kwa namna hiyo fedha hiyo itawanufaisha watu wa kipato cha chini vijijini kwetu. Hata kila jimbo likipata mipira 100 na seti kadhaa za jezi tu itasaidia sana kwa kuanzia.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia hoja ya Wizara ya Maji. Kwanza nianze kwa kutoa shukrani kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara nzima kwa ujumla. Natambua hivi karibuni ulitembelea mradi wa maji wa Kilolo, Isimani mradi ambao unaendelea na uko asilimia zaidi ya 30 na ninaamini utakamilika. Pia ninaendelea kushukuru kwa sababu ya ukamilishaji wa mradi wa maji ya Ilula ambao ulikamilika kipindi kile kilichopita na nimeshautaja huo mradi huko siku za nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikija kwenye kuchangia, kwanza nianze kwa kutoa ushauri mdogo. Kuna baadhi ya mashirika ambayo yanatoa huduma za maji, lakini siyo kupitia mfumo wa Serikali. Kama pale Iringa, nafahamu kuna shirika linaitwa Waridi na wamefanya kazi nzuri tu, lakini pia sehemu nyingine nchini yapo mashirika kama hayo. Mimi nashauri kuwe na mfumo wa uratibu ili tujue, kwa sababu wakati mwingine ile miradi wakishaijenga wanaondoka. Wakiondoka kwa sababu haikuwa kwenye mfumo wa Idara za Maji, unakuta wakati mwingine nayo inakufa kama wengine walivyosema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ushauri wangu, tungefanya tathmini ya miradi ambayo imefadhiliwa na watu wengine nje ya mfumo wa Serikali, lakini inafanya vizuri ili iweze kuingizwa kwenye mfumo wa usimamizi na ufuatiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nikijikita kwenye eneo la Kilolo yenyewe, jambo la kwanza nakuomba kupitia kiti chako, naomba Mheshimiwa Waziri aangalie ule mradi wa maji wa Ilula ambao nimeutaja, kwamba ulijengwa na maji yamefika pale, lakini usambazaji bado haujafanyika. Kwa hiyo, watu wanaweza kwanza kwenda kuchota kwenye tanki, inakuwa ni kitu kile kile. Mimi natamani sana kungepatikana fedha ili usambazaji ule ufanyike kupitia mifumo ya maji ile na kuondoa kabisa upotevu wa maji ambao kama tukitumia mifumo ile ya zamani sana, maji yale yatapotea na hayatawafikia walengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuongezea, ule mradi unasimamiwa na IRUWASA na sasa RUWASA wana Kata za pembezoni ambazo zinaweza kunufaika. Napendekeza kuwe na mazungumzo kati ya IRUWASA na RUWASA ili Kata kama ya Uhambingeto ambayo iko pale karibu iweze kuchukua maji kutoka kwenye ule mradi. Hili nimeshalifikisha kwa viongozi wa IRUWASA na RUWASA Mkoa na nina hakika ukiwekwa msisitizo, basi litafanyika kwa haraka zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ipo miradi mingine ambayo inaendelea ambayo ningependa kuitaja. Kuna mradi mdogo wa maji wa kule Kata ya Kimala. Huu mradi ulianzishwa na wananchi wenyewe kwa nguvu zao na unaendelea vizuri na haya maeneo ya milimani, ndiyo ile mnaanza kusema wakati mwingine Iringa kuna udumavu. Ni kuchota maji, kwa sababu ni milima, watu wanaposhuka na kupanda na wamebeba madumu, yanawakandamiza, kwa hiyo, wanashindwa kurefuka. Kama utafiti ukifanyika,0 utaona kwamba uchotaji maji kwenye milima unasababisha watu wafikiriwe kuwa wadumavu au wafupi. Ni aghalabu kukuta watu watu warefu kwenye maeneo hayo kwa sababu ya uchotaji wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata kama ya Kimala, hiyo inatatizo ya maji na wameanzisha wananchi wenyewe ule mradi. Ili utunusuru tuweze kurefuka, tunakusihi Mheshimwa Waziri, tafadhali ule mradi wa maji uweze kukamilishwa pale Kata ya Kimala. utahudumia...

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nyamoga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumpa taarifa mzungumzaji kwamba Mkoa wa Iringa na baadhi ya Mikoa mingine inajulikana kwa udumavu ambao unatokana na mambo ya lishe. Sasa akiongea kama Mbunge, akasema ni udumavu wa kubeba maji tu, atakuwa anapotosha hata na ile elimu ya kutoa kule chini ili watu wetu waweze kuendana lishe bora watake, kuachana na udumavu. Inawezekana waliokuwa na udumavu wa juu, yaani baada ya kubeba, ni shingo tu, lakini hudumavu wa Iringa ni wa ukosefu wa lishe bora kwa wananchi wetu. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Justin Nyamoga, unapokea taarifa hiyo?

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, utafiti ukifanyika utadhibitisha kama kuchota maji na kubeba, kunaweza kusababisha mtu kuwa mfupi au kurefuka. Kwa hiyo, siipokei kwa sababu utafiti bado haujafanyika.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Justin ngoja niliweke vizuri. Mtu mfupi haimaanishi ana udumavu, lazima tuwe tumeelewa vizuri. Ufupi hauna uhusiano na udumavu, kwa sababu hata mtu anaweza kuwa ni mrefu na akawa na udumavu. Kwa hiyo, tutofautishe jamani, hayo ni mambo ya kisayansi. Udumavu ni ukosefu wa chakula katika umri fulani hivi; chakula bora, ama lishe bora. Mimi mwenyewe nimeshabeba ndoo Mheshimiwa usiwe na wasiwasi. (Kicheko)

Mheshimiwa Justin Nyamoga, malizia mchango wako.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba niendelee kuchangia. Kwa hiyo, kuna hiyo Kata ya Kimala, lakini pia kuna Kata ya Ukwega, Vijiji vya Mkalanga, Makungu, Uinome, Lukani, vyote hivyo bado havijafikiwa na vina miradi midogo midogo ya maji ambayo ningependa ikamilishwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mradi ambayo inahitaji kukarabatiwa. Hii ni ile miradi unayokuta ina ukarabati, na nimeiona kwenye bajeti, nashukuru; mradi kama pale Kitoo, Mradi wa Ihimbo, Magana Ilindi na Mradi wa Kipaduka. Hiyo ni miradi ambayo ipo; na miradi ya kule mingi, kwa sababu vyanzo vinapatikana, kwa hiyo, siyo miradi mikubwa kwa sababu ni chanzo, halafu maji yake yanatumia gravity, ambapo kwa kawaida ukarabati wake siyo wa gharama. Kwa hiyo, napenda miradi yote ile iliyopo kwenye Jimbo la Kilolo iweze kuangaliwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile kuna mradi mkubwa. Ule mji wa Kilolo unakua na ninajua kwamba Mji wa Kilolo hauko kwenye miji 28. Miji hii ambayo wilaya zinaanzishwa ikiwa ni vijiji, inapokua kwa kasi halafu hatuweki miundombinu ya maji, kawaida baadaye tunapata shida ya maji. Kuna pendekezo limeletwa na IRUWASA la Mradi wa Mto Mtitu na limeshapokelewa kwenye Wizara yako; naomba mradi ule kwa sababu ni mkubwa na utakidhi mahitaji siyo ya Jimbo la Kilolo tu, unaenda pia kwa baadhi ya maeneo ya Jimbo la Kalenga na unafika hata katika Jimbo la Iringa mjini. Nasihi ule mradi uweze kuangaliwa kwenye Mfuko wa Maji ili uweze kufanya kazi katika maeneo hayo na wale watu waweze kutua akina mama ndoo kichwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba suala zima la kumtua mama ndoo kichwani ni la muhimu sana kwenye Jimbo la Kilolo kama nilivyosema. Nimesema kwa kuzingatia sana suala la maeneo yenye miinuko la milima na maji yanakuwa chini, ndiyo maana nilizungumzia kuhusu kupanda na kushuka kila siku; na nimeshangaa Mheshimiwa Naibu Spika, kama nawe ulibeba ndoo na ukaweza kuwa na kimo hicho, lakini kwetu sisi haifikii hivyo mara nyingi. Nami nasema utafiti ukifanyika, tumebeba sana maji, ndiyo maana tunakuwa hivi. Kwa kuwa sasa tuna Waziri makini, nina hakika wananchi wa Kilolo hasa wale wa maeneo ya milimani wataungana nami kwamba baada ya kuacha kubeba maji na baada ya hili tatizo kwisha, tutakuwa nasi tunapata nafuu kidogo au ahueni hata ya kurefuka ili tuweze kuwa kama Watanzania wengine. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya hayo, naunga mkono hoja ili hii bajeti iweze kupita na wananchi wa Kilolo waweze kupata maji. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa fursa hii ili niweze kuchangia Wizara hii muhimu ya Ujenzi na nitajikita zaidi katika maeneo mbalimbali ya Jimbo la Kilolo jimbo ambalo ni pendwa sana kwa upande wangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla sijaanza kuchangia kiundani nataka nitoe tu mlinganisho wa bei za vitu unaotokana na ubovu wa miundombinu katika eneo la Kilolo. Mfano, ubao wa mbili kwa nne unaouzwa Sh.6,000 Mafinga, Kilolo utauzwa kwa Sh.3,500 na hii ni kutokana na changamoto za miundombinu ya usafirishaji. Sasa Barabara hii ya kutoka Iringa Mjini kwenda Kilolo hadi Idete ni barabara ambayo ni ahadi za Maraisi kadhaa kama zilivyo barabara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kwa kiasi fulani nianze kuipongeza Wizara kwa kazi ambayo tayari inafanyika. Najua kuna kilometa 10 ambazo mkandarasi yupo kazini, amekuwa taratibu kidogo, huyu mkandarasi amefanya kazi pale kwa karibu miaka mitatu, nimepita hivi karibuni nimeona sasa angalau kazi inaendelea, inatia moyo. Nafahamu pia kwamba kuna kilometa tatu nyingine za kutoka kwenye daraja pale Ndiwili kuelekea mjini ambazo zimeshapata makandarasi, nalo pia ninalipongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tutakuwa tumebakiza kama kilometa 13 hivi kufika Iringa Mjini, naomba, nimeona imetengwa shilingi 140, sijajua milioni 140 ni ya kilometa ngapi, lakini imeandikwa kwamba ni kuweka lami kwa hizo kilometa zilizobaki, basi naomba kama ambavyo barabara nyingine zina umuhimu, hii milioni 140 iongezewe ili ile barabara iweze kufika Iringa Mjini. Hiyo ndiyo wilaya peke yake kwenye Mkoa wa Iringa ambayo haijaunganishwa na barabara ya lami hadi kwenye Makao Makuu ya Mkoa. Kwa hiyo kama tutakamilisha hiyo, nitakuwa na sababu ya kupongeza na nitakuwa naunga mkono hoja zenu kwa moyo mkunjufu kwenye miaka ijayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia nizungumzie kuhusu hii barabara ambayo inatoka Ilula inapita Mlafu inaenda Ukwega - Kising’a - Mtitu na inakuja kutokea Kilolo ambayo uchumi wake ni mkubwa na tayari kutokana na athari za mvua barabara hii inapitika kwa shida sana. Kwanza inatakiwa ifanyiwe maintenance ya kawaida kabla haijawekwa lami, lakini mapendekezo yangu, kwa sababu barabara hii inasumbua mara nyingi kwenye maeneo kadhaa na kwa sababu tayari Meneja wa TANROADS ameshafanya ubunifu wa kukata baadhi ya milima ili barabara ile iweze kupitika kwa urahisi jambo ambalo tunapongeza. Ningependa yale maeneo ambayo yana hali ngumu zaidi yanapitika kwa shida na yale maeneo mbayo udongo wake ni shida hata ukiweka kokoto inazama yale yafikiriwe kuwekwa lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuwe na mpango wa kuweka lami katika maeneo korofi, sisi hatusemi muweke yote, sisi tunasema waweke maeneo korofi, wakitupa kilometa mbili tutachagua sehemu ya kuweka, wakitupa kilometa tatu tutachagua sehemu ya kuweka, ili mradi magari yaweze kupita kwa muda wote. Kule sasa hivi kuna watu wengi ambao ni wazawa wanaoitwa wawekezaji, wanafanya kilimo cha maparachichi na tayari wameshaanza kuuza. Njombe bei ni kubwa kule sasa hivi wanauza kilo moja ni Sh.1,000, tatizo ni miundombinu ya barabara hiyo ambayo ni barabara inayokatisha kwenye eneo kubwa sana la Jimbo la Kilolo na ni barabara ya muhimu. Naomba barabara hii itiliwe mkazo hasa kwenye maintenance na kwenye kuweka lami kwenye maeneo korofi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ningependa kujielekeza, ni kuhusu utaratibu wa kupaki magari hasa Ilula na Ruaha Mbuyuni. Sasa hivi pale Ilula kimewekwa kituo nafikiri ni cha watu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, sasa wameweka banda pembeni ya barabara na magari sasa yanapaki pale yanaziba ile barabara kabisa. Nafikiria hizi sehemu kama Ilula ambapo kunahitajika ile barabara iwe wazi, basi kama kunawekwa kituo chochote cha kiserikali kitafute namna nzuri kama ilivyofanywa mizani. badala ya kuweka stop ambazo zinazuia barabara hasa kwenye haya maeneo. Tatizo hilo linaweza likawepo hata kwenye maeneo mengine, lakini kwa uchache nitayataja hayo maeneo mawili Ilula na Ruaha Mbuyuni ambayo nimepita na kuona na kuona kwamba ile ni changamoto kubwa na ningefikiria kwamba ingeweza kufanyiwa marekebisho ili magari yaweze kupita kwa urahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa pia kutaja eneo lingine ambalo kama lingekarabatiwa vizuri lingetusaidia. Barabara hii kutoka pale Kidabaga kuna milima michache, kuna Mlima Msonza uko pale, wenyewe huko nyuma ulikuwa haupitiki kabisa, lakini baada ya ukarabati
ule mkubwa unapitika, lakini ile mifereji ile miundombinu yake kwa sababu milima ya kule inamomonyoka, Serikali inatumia fedha nyingi sana kuchimba ile milima, lakini kwa sababu hakuna namna yoyote inayowekwa ili kuzuia ile milima isimomonyoke ile milima inaendelea kumomonyoka na kuharibu tena barabara. Kwa hiyo kuna namna ya kutengeneza ile miundombinu ya mifereji ili barabara zile ziendelee kudumu kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zile sehemu zote pia hapo kwenye Mlima Msonza ukienda kama unaenda Idete kuna milima mingine kama miwili, ile nayo kwasababu ni milima ambayo ni sumbufu kwa muda mrefu na yenyewe ingeweza kufikiriwa kuwekwa lami. Tunapozungumzia lami hatuzungumzii, sisi hata ingewekwa kama hii ambayo ni ya kwenda Iringa iliyochanikachanika hata ikimwagiwa kokoto kokoto tu sisi hatuna tatizo ili mradi iweze kupitika mwaka wote. Kwa sababu sisi hatutajali sana ubora ili mradi ipitike tu mwaka mzima, nafikiri hapo hata bei itakuwa nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hizi milioni 60 walizotuwekea, milioni 140 wakiongeza tu kama milioni 300 hivi angalau tutapata kilometa saba au nane zitasaida katika yale maeneo ili wananchi waweze kupita kwa urahisi na waendelee vizuri na shughuli zao za kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili niweze kuweka mkazo kwenye hizi barabara ambazo nimezitaja labda niendelee kuweka msisisitizo zaidi kwenye kipengele cha barabara nyingine ambazo zipo katika Mkoa wa Iringa na niza kiuchumi na kwa kweli tulikubaliana katika Mkoa wa Iringa kuendelea kuzitaja hasa zinazoingia kwenye mbuga za Wanyama. Na hapa nataka nikumbushe kwamba mbuga ya wanyama ya Udzungwa ambayo kwa kiwango kikubwa iko katika Wilaya ya Kilolo asilimia 80 lango lake la kuingilia liko Morogoro ambako ni asilimia 20 tu ya mbuga ndiko iliko na hii inatokana na tatizo la miundo mbinu la barabara inayotokea pale Mahenge na kuingia Udekwa ambapo kuna geti ambalo ndiko asilimia 80 ilipo. (Makofi)


Mheshimiwa Naibu Spika, na hii barabara ilishachimbwa kilomita 14 lakini haikutoboka kwa hiyo walianzia Udekwa wakachimba kilomita 14 wakaitengeneza tu vizuri kabisa lakini imebaki kilomita 7 kuingia kwenye lami. Sasa kule kunaota majani huku walikochimba kilomita 14 ni useless kwa sababu hakuna mtu anayepita kwenda asikofika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ningependekeza pia kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili ambako ndiko geti liliko lile geti la Udekwa waweze kwenda kuangalia kama ilikuwa ni halali kuchimba barabara na kuacha kilomita 7 kutoboa kwenye barabara ya lami halafu unaishia hapo halafu ile barabara inakuwa yakwenda porini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, sasa hivi wanapita tu Ngedere Tumbili na wanyama wengine waliopo kule, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia hoja hii ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kupongeza kazi nzuri ambayo inafanyika hasa ya usambazaji wa umeme katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Katika jimbo langu ni kweli kumekuwa na utekelezaji mzuri sana kwenye awamu hizo zilizopita hadi maeneo ambayo kwa kweli ni ya mbali sana na kwa sababu eneo langu ni la milima, Kata kama zile za Kimala, Idete na Masisiwe, nyaya na mita zimefungwa lakini umeme bado haujawashwa. Nimeshamwambia Mheshimiwa Waziri baada tu ya kumaliza bajeti hii twende naye kwa sababu wakimuona najua kabisa umeme utawaka kwenye kata zile. Kwa hiyo, naamini kwamba yuko tayari na tutaongozana na kwa sababu nimeona dalili kwamba baada tu ya kuwa nimeongeaongea watakuwa wanaendelea kuhakikisha kwamba wanakamilisha wakijua ziara yako inakaribia. Kwa hiyo, Kata hizi za Kimala, Idete na Masisiwe tunamsubiri kwa hamu ili umeme uweze kuwaka.

Mheshimiwa Spika, lakini bado kuna kata tatu nzima ambazo hazijafikiwa na umeme. Kuna Kata nzima za Nyanzwa, Ukwega na Udekwa. Kwa mfano, Kata ya Ukwega kwenye Kijiji kile cha Ipalamwa kuna kituo cha afya kimejengwa kwa hisani lakini hakiwezi kufanya upasuaji hata kama wana vifaa kwa sababu hakuna umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo mengi niliyoyataja haya tayari kuna kilimo kikubwa sana cha parachichi na watu wameshaanza kujenga majengo kwa ajili ya kuhifadhia mazao yale ambayo yanahitaji umeme. Kwa hiyo, naamini kwamba atakapokuwa ameshafikisha umeme kule basi shughuli za kiuchumi zitaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, napenda nimkumbushe Mheshimiwa Waziri nimeshaongea naye pamoja na Naibu Waziri; pale kwenye Kijiji cha Kipaduka, Kata ya Wambingeto ambapo kulikuwa na mradi ulipeleka pale transfoma, nguzo zipo, transfoma ile iko kwenye ofisi za kijiji kwa muda mrefu na tatizo ni kwamba kuna afisa mmoja huko hajatoa kibali ili REA iweze kufanya kazi ile. Wale watu wa Kipaduka wamekaa na zile transfoma kwenye ofisi ya kijiji muda mrefu mno, hawawezi hata kujua wafanye nini basi naomba yule anayetoa kibali kama yuko hapa kwa sababu najua maafisa wenu wanahudhuria akumbuke kutoa hicho kibali ili pale Kipaduka hilo tatizo liweze kuisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kutaja pia Kata ya Ilole, kwenye Kijiji hichohicho cha Ilole kuna tatizo kwamba umeme haujafika na hakimo kwenye orodha ya vijiji ambavyo havijapatiwa umeme. Kwa hiyo, naomba nacho kiongezwe ili vijiji vile ambavyo havijapata umeme viweze kufika 22 vikiwa ni pamoja na Vijiji vingine kama Muhanga, Idunda na Ibofwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie kwa kuzungumzia suala la hifadhi ya mazingira, hasa kwa sababu Jimbo la Kilolo ni jimbo ambalo ndilo linalotoa maji mengi yanayotiririka kwa ajili ya Bwawa la Mtera.

Naomba kutoa angalizo hili kwa sababu tunajua kwamba umeme wa maji bila kuhifadhi haya mazingira inawezekana ikafika wakati tukakosa maji. Kwa sababu najua Waziri anayehusika na mambo ya mazingira yuko hapa pia, napenda kuhimiza kwamba ni suala la kuliangalia kwa sababu katika maeneo haya kuna kilimo kinaendelea kama tusipopanga vizuri na tukaweka hifadhi ya mazingira vizuri, basi upo uwezekano baadaye kuja kukosa maji. Hii inategemea na ufadhili wa miradi iliyomo pembezoni mwa mito na hasa vile vijiji ambavyo maji yanatiririka kuelekea kwenye hilo eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, katika Wizara hii naomba kuchangia kama ifuatavyo; kwanza Wizara inatakiwa kuangalia uwezekano wa namna ya kunufaika na miradi ya kupunguza hewa ya ukaa iliyopo duniani ambayo wapo baadhi ya wawekezaji wameanza kuwekeza nchini, tunayo misitu ya asili mingi ambayo kwa maoni yangu inakidhi vigezo vya kulipwa fidia.

Mheshimiwa Spika, pili, kutenga bajeti ya kutosha kwa ajili ya Wilaya zenye vyanzo vingi vya maji kama Wilaya ya Kilolo ili kuendelea kulinda vyanzo hivyo na kuwa na njia mbadala za kiuchumi ambazo ni rafiki kwa mazingira.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, napongeza sana Wizara kwa kazi nzuri ya kuboresha mitaala; ushauri wangu ni kuhusu kuzingatia na kutafuta njia nzuri ya udhibiti ubora kwa shule zilizopo nchini lakini zinatumia mitaala ya nchi nyingine. Shule hizi zinazidi kuongezeka lakini udhibiti wake ni mdogo na kuna dalili za uholela katika uanzishwaji na usimamizi wake hivyo kuathiri ubora katika utoaji wa elimu katika shule hizo. Mfano ni shule zinazotumia mtaala wa Cambridge.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili naomba sana Wizara isikie kilio chetu cha Jimbo la Kilolo kujengewa Chuo cha VETA. Tayari eneo tunalo na wananchi na halmashauri tupo tayari kushirikiana katika kuhakikisha chuo hicho kinajengwa.
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote na mimi nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Hoja ya Kamati na nitajielekeza zaidi kwenye Kamati ya Bunge ya Kudumu ya TAMISEMI. Ninamshukuru na kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya hasa kwa uwekezaji wa fedha nyingi sana kwenye miradi ya maendeleo katika halmashauri za nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifano ipo mingi, shule za sekondari za mikoa, kila mkoa fedha zimepelekwa na ujenzi unaendelea lakini kupitia SEQUIP kila halmashauri inaendelea kupokea fedha kwa ajili ya ujenzi wa shule; lakini wote tunaona miundombinu ya afya pamoja na vituo vya afya pamoja na hospitali na vifaatiba vimepelekwa kwa wingi. Kwa kweli kazi inafanyika na naamini kabisa mwenye macho haambiwi tazama, tunaona mambo megi ambayo yanafanyika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nichukue nafasi hii pia kumshukuru na kumpongeza Waziri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI pamoja na Manaibu Mawaziri na Makatibu Wakuu kwa ushirikiano mkubwa wanaoendelea kuonyesha katika utekelezaji wa kazi hizo kwenye maeneo mbalimbali tunapoendelea kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye maoni na mapendekezo mbalimbali ambayo yamefanywa na Kamati ya TAMISEMI hasa kwenye upande wa eneo la TARURA. Barabara ni siasa kubwa kwenye nchi yetu hasa maeneo ya vijijini na hali tuliyonayo kwa sasa ni mbaya hasa baada ya kipindi hiki cha mvua. TARURA ilitengewe shilingi bilioni 818, hivi tunavyozungumza zilizoenda ni bilioni 82 tu ambayo ni sawa na asilimia 12, ndiyo fedha zilizopokelewa. Maana yake ni kwamba kuna fedha zaidi ya asilimia 80 ambazo hazijapelekwa na sasa tuko kwenye kipindi ambacho tunaelekea kumalizia mwaka wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata kabla hatujazungumzia ongezeko la bajeti kutoka hii milioni 800 kwenda trilioni 1.6, hizi fedha ambazo mwaka huu zilitengwa, tunaiomba Serikali na tumeiweka kwenye maazimio ipeleke fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara, fedha ambazo zilikuwepo kwenye bajeti iliyopita; na kwenye azimio hili tumesisitiza sana Wizara ya Fedha kuweka vipaumbele vyake sawa sawa kwa sababu hatuoni kipaumbele kikubwa kwa sasa hivi cha dharura zaidi ya miundombinu ya barabara. Kwenye maeneo mbalimbali ya vijijini, akina mama wanakufa kutokana na kushindwa kusafirisha wagonjwa kwenye maeneo hayo. Mazao yanaoza kwa sababu hatuwezi kusafirisha mazao katika kipindi hiki ambacho barabara zimekatika na kuharibika na changamoto mbalimbali zinazotokana na miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hatujajua Wizara ya Fedha ina kipaumbele gani kingine kikubwa zaidi ya miundombinu ya barabara kwa sasa, hadi kusababisha fedha asilimia 12 tu ya bajeti ipelekwe hadi kufikia Desemba, ambapo ni nusu ya mwaka, ambapo tulitarajia fedha ambayo imepelekwa ingekuwa angalau zaidi ya asilima 50. Kwenye azimio letu hili lipo na naomba Bunge likubali kuazimia jambo hili lakini baada ya kuazimiwa jambo hili litekelezwe na Wizara ya Fedha mara moja kwa kuipa TARURA fedha ili iweze kutekeleza majukumu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la elimu yako mambo mawili ya muhimu pamoja na ujenzi wa miundombinu mizuri, halmashauri zimepokea fedha nyingi sana kutoka Serikali Kuu na kwa sababu zimepokea fedha nyingi sana kutoka Serikali Kuu na ujenzi wa madarasa umefanyika vizuri kuna changamoto mbili. Kwanza ni madawati lakini pili ni miundombinu ya vyoo kwenye shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa halmashauri zimekwisha kusaidiwa ni muhimu sasa TAMISEMI kuangalia halmashauri zote kuja na mkakati wa kumaliza tatizo la madawati kwa kupitia mapato ya ndani kwa sababu tayari wameshasaidiwa madawati; kwa sababu tayari wameshasaidiwa miundombinu ya madarasa. Kwa hiyo katika eneo hili, katika bajeti ijayo miundombinu ya vyoo pamoja na madawati iwe ni kipaumbele kwenye sekta ya elimu kwa sababu kama madarasa ni mazuri basi na miundombinu ya vyoo iwe mizuri na madawati yawepo ili watoto wetu waendelee kuwa kwenye mazingira mazuri ya elimu na waweze kuendelea na masomo vizuri. Hili pia tumeliweka kwenye maazimio na nina hakika Bunge litaazimia na kupitisha ili liweze kutekelezwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mwenyekiti wa Kamati ya TAMISEMI anawasilisha aliataja suala la halmashauri mbalimbali kujifunza kuhusu kutunza misitu ya asili kwa ajili ya uvunaji wa hewa ya ukaa. Ningependa kutoa mfano mmoja wa Halmashauri ya Kilolo, Hifadhi tu za misitu ya Kijiji, Halmashauri ya Kilolo ni hekta 50,531 lakini hapo nimeacha kutaja hekta za TFS ambazo ni 198.599. Ninaamini hii ni moja kati ya halmashauri zenye eneo kubwa sana la hifadhi ya misitu ya asili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale TAMISEMI kuna kitengo nafikiria au idara kuna mtu anashughulika na kuanzisha hii miradi ya uvunaji ya hewa ya ukaa na kuna halmashauri nyingi ambazo zingeweza kukusanya mapato zaidi ya mapato yake ya ndani kwa kupata fedha kutokana na uvunaji wa hewa ya ukaa na tayari kuna halmashauri chache zimeshaanza kunufaika. Tunachojiuliza ni nini kinachelewesha TAMISEMI pamoja na Ofisi ya Makamu wa Rais, Wizara ya Mazingira kuwekeza katika kuhakikisha kwamba halmashauri zote zenye misitu ya asili zinaingia kwenye uvunaji wa hewa ya ukaa ili kujiongezea mapato, kwa sababu jambo hili lingeweza kupunguza sana gharama za unedeshaji wa halmashauri kwa kutoa fedha kwenye Serikali Kuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hii jambo limetajwa pale kwenye taarifa yetu na tunasisitiza na kuiomba TAMISEMI pamoja na Wizara ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira na Muungano kuliangalia na kuangalia ni mkakati upi unaweza ukafanywa ili halmashauri zote zenye misitu ya asili na imezitunza kuweza kuingia kwenye uvunaji wa hewa ya ukaa kwa kufuata miongozo ilipo. Ni kwa nini halmashauri chache zipate mabilioni ya pesa na halmashauri zenye misitu mikubwa kuliko hata hizo zinazopata zenyewe hazijaanza. Ni nini kipo hapo? Na kwa nini hakiwezi kutatuliwa? hilo tungeomba liweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoelekea kumalizia nitaje mambo mawili ya muhimu. La kwanza ni suala zima la kuwa na mwongozo mzuri wa posho za viongozi katika ngazi za vijiji na ngazi ya kata, hasa kwa sababu kwa sasa kuna halmashauri nyingi viongozi hao hawapati posho zozote. Kwa hiyo ni lazima tuwe na mwongozo …
MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: …ili viongozi hao waweze kupata posho katika…

MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: …kwa kufuata mwongozo uliotolewa na TAMISEMI. Kwa sasa inakua ni changamoto kubwa kwa sababu…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Lazaro…

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: …hakuna mwongozo wowote…

TAARIFA

MWENYEKITI: Kuna taarifa kwa Jirani yako.

MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa Kaka yangu mchangiaji, kwanza Serikali yetu ya Awamu ya Sita chini ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan iliridhia kabisa Watendaji wa Kata waweze kupewa posho za madaraka, lakini pamoja na hiyo sambamba na hivyo halmashauri nyingi hawawapi posho za madaraka kwa wakati.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Justin Lazaro, taarifa unaipokea? Malizia mchango wako.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea na kuongezea tu pamoja na hilo kwa sababu ni muda mrefu umepita, madiwani pia posho zao hazijafanyiwa mapatio. Kwa hiyo tunatarajia kwenye bajeti ijayo Serikali italeta mapendekezo ya nyongeza ya posho za madiwani lakini na mwongozo mzuri wa ulipaji wa posho kwa viongozi wa ngazi za vijiji na viongozi wa ngazi za vitongoji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja zote mbili, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa muda huu ili niweze kuchangia hoja hii muhimu ya Wizara ya Maliasili na Utalii.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kwanza, niungane na wenzangu kupongeza kazi nzuri inayofanyika na Wizara hii, Waziri, Naibu Waziri pamoja na watendaji wake pamoja na Kamati kwa ujumla, bajeti iliyoletwa na mapendekezo yote ni mazuri kabisa, nawaponga sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wangu, jambo la kwanza, napenda nikumbushe nililizungumza hili wakati nilipochangia Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi. Ile Mbuga ya Udzungwa asilimia 80 ipo Wilaya ya Kilolo na hilo Wizara inalifahamu. Jambo la kwanza, hakuna geti hata moja la kuingia Mbuga ya Udzungwa kwa Wilaya ya Kilolo ambako ndiko asilimia 80 ilipo. Zile ofisi za TANAPA zilizopo pale Udekwa, barabara yake haijajengwa na nilisema hapa kwamba, walianzia kule Udekwa kuja pale Mahenge kwenye barabara ya lami. Wakatengeneza kilomita 14 kwenda barabarani ikaishia porini bado kilomita saba.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua kwamba, Wizara hii na TANAPA kwa sababu, ofisi zao ziko pale Udekwa hatuwezi kushindwa kutengeneza zile kilomita saba ili tuingie kwenye zile ofisi zao na pia ili tuweze kulifikia lile geti, kwa sababu, kwa sasa tunazunguka karibu kilomita 60 mahali ambapo tungetumia kilomita 20 kufika pale kwenye lile geti na ile barabara ya kilomita 60 yenyewe si nzuri. Kwa hiyo, napendekeza kwamba, kwa pamoja mimi niko tayari kushirikiana hata na wananchi, tutoboe ile barabara na yenyewe tutafute fedha kidogo tuweke greda tumwage kokoto, hatusemi lami lakini ifike kwenye lile geti, angalau tuwe na geti moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yake ni kwamba, Mbuga ya Udzungwa hiyo inayotumika ni asilimia 20 tu kwa sababu, kule kote kumebaki pori, asilimia 80 ya mbuga haitumiki, jambo ambalo ningependa tushirikiane ili tufungue na kama kuna haja ya kuongeza mageti mengine tuongeze, kwasababu, ile ni Mbuga kubwa na ina maeneo mengi, ambayo yangeweza kuwa na vivutio.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo kwa unyenyekevu sana, naomba Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wanisikilize kwa sababu hii ni changamoto ya kipekee. Katika Kata ya Kidabaga, Kata ya Masisiwe na kidogo Kata ya Ng’ang’ange kuna changamoto ya ngedere na wale ngedere wanatoka kwenye ule mpaka na ni wengi. Wale ngedere wanavuna mahindi kama ya kwao na kuna usemi usemao ukicheka na ngedere au nyani utavuna mabua, wale watu kule sasa hivi wanashinda kule porini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilienda kwenye mikutano, watu wanafanya zamu, natakiwa niwe na mikutano miwili wa asubuhi ili wengine wahamie ngedere na wa mchana ili wengine waende warudi. Wale ngedere sio kivutio kwa sababu, kuna baadhi ya wawekezaji kule wanatoka hata Ulaya, lakini nao wanalalamika. Ngedere wale wanakula wakimaliza wanakaa hata kwenye shule za msingi na wanafanya burudani zao nyingine siwezi kusema hapa. (Makofi/Kicheko)

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, Taarifa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kitolewe kibali wavunwe. Kama kuna mahali wanaliwa wakavunwe waliwe, kwa sababu, ni wengi na wanazaliana sana. Ni changamoto kubwa sana na ningependa itatuliwe.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Nyamoga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kumpa taarifa mzungumzaji kwamba, ifike wakati sasa watu wa Maliasili waangalie, kama wenzetu hapa wachina hivi vitu vyote wanakula? Kwa nini bucha za ngedere, nyani na vitu vingine zisiwepo? Ili hao watu waje wanunue hizo nyama wapeleke huko? (Makofi)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kuzungumzia suala la tembo pale Kata ya Nyanzwa pamoja na Kata ya Ruaha Mbuyuni. Kwa sasa kwa mwaka huu tu wamekufa watu 12, Kata ya Nyanzwa nane na Ruaha Mbuyuni wawili, tayari wameshauawa. Huenda nao ni ushoroba, lakini kwa kweli ni changamoto kubwa na naomba Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri wakimaliza hapa, twende pale, wameweka askari pale wanalima vitunguu tu. Tena wakati tembo akiua mtu, wanataka wananchi wachange fedha. Sasa tembo ameshaua watu wakae vikao, wachange fedha wakakodi gari ndipo wakawachukue, ndipo waende wakawaue au wakawafukuze hao Tembo.

NAIBU SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, inachukua muda mrefu sana nawaombeni sana haya.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli naomba Wizara wayafanyie kazi hayo. Hata hivyo, naunga mkono hoja, ikiwa hayo niliyosema yatazingatiwa. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Kilolo kuna mwekezaji anaitwa Udzungwa Corridor ambaye anawekeza katika kupanda miti ya asili kwa ajili ya uvunaji wa hewa ya ukaa. Shida iliyopo ni ukiukwaji wa taratibu za umiliki ardhi na uwazi katika uwekezaji huo. Naiomba Wizara ije na majibu je, inamfahamu mwekezaji huyu? Kuna haja ya Wizara kushirikiana na Halmashauri kuona ni jinsi gani mwekezaji huyu ataheshimu mikataba yake na wananchi na kuacha kununua maeneo ya wananchi wanayoyatumia kwa shughuli za kilimo. Mwekezaji huyu amenunua hadi eneo la ujenzi wa shule ya sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili; Kilolo ina misitu mingi ya asili kuna haja ya Wizara kutoa support kwa Halmashauri ili kuanza uwekezaji.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi hii niliyopewa ya kuchangia. Nianze kwa kumshukuru Mungu kwa nafasi hii kwa kusoma mstari wa Zaburi ya 136:1 katika Biblia, unasema; “Mshukuruni Bwana kwa kuwa ni mwema, kwa maana Fadhili zake ni za milele.” (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza ninapenda sana kuipongeza Serikali kwa ujumla, hasa Mheshimiwa Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya pamoja na Mawaziri wote, pamoja na Waziri wa Fedha kwa bajeti nzuri sana ambayo imewekwa mezani petu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti hii inatoa matumaini makubwa kwa Watanzania pamoja na Wanakilolo ambao kwa kuiangalia tu tayari tumeshaanza kupata matunda ya Awamu ya Sita kwa zile milioni 500, tumeshazipokea kwa ajili ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunajua tunakaribia kupokea shilingi milioni 600 kwa ajili ya shule za sekondari. Yote hayo tunajua ni juhudi ambazo zinafanyika katika kulikwamua Taifa letu, likiwemo Jimbo la Kilolo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi nimesikiliza hotuba ya Mheshimiwa Rais, nami nikaitafakari wakati alipokuwa akiongea na vijana. Tafakari yangu hasa ililenga kwenye kuwawezesha vijana kimitaji. Mheshimiwa Rais amekuja na wazo zuri sana la kuanzisha benki ya vijana. Hapa niliona ni vema nikatoa ushauri wangu. Ushauri huu unatokana na haya yafuatayo:- (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo benki mbalimbali zilizoanzishwa kwa malengo maalum. National Microfinance Bank (NMB), hata kwa maneno yake, ni benki ya mikopo midogo midogo (microfinance). Tunayo Mwalimu Commercial Bank iliyoanzishwa kwa ajili ya walimu. Vile vile tulikuwa na Tanzania Women Bank. Kinachozitesa hizi benki ni riba. Kama riba ingekuwa ndogo, hatuhitaji kuanzisha benki nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anafahamu, tuna benki zenye mtandao nchi nzima. Hizi benki nilizozitaja zote zilikuwa Dar es Salaam, kama zimeenda mbali sana, zitakuwa Arusha au mahali pengine katikati ya miji. Tunazo benki zilizosambaa mahali pote. Pendekezo langu na ambalo nafikiri ningeweza kushauri ni kuanzisha madirisha maalum kwenye benki ambazo hata Kilolo zipo, lakini riba isiwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafahamu kwamba kama kuna fedha kwa ajili ya kuanzisha hii benki, hatutawekeza kwenye kodi ya majengo, hatutawekeza kwenye miundombinu, hata wafanyakazi hatutawekeza, tayari wapo. Tuangalie benki ambazo tayari zina mitandao ili vijana hata kesho kama hiyo hela ipo ikiwekwa, wafundishwe hao wafanyakazi kwenye hizo benki ambazo zipo tayari ili vijana waweze kupata mikopo na waweze kufanyakazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, masharti katika benki pia yakipunguzwa, hawa vijana hata hii benki ikianzishwa kama wataambiwa wapeleke collateral ya nyumba, hawana. Kama wataambiwa wapeleke collateral ya viwanja, hawana. Kwa hiyo, kinachowatesa siyo benki, ni riba na masharti ya hizo benki. Kama likianzishwa dirisha maalum na hilo dirisha likaondoa hayo masharti, basi kazi itakuwa rahisi sana kuwawezesha vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuongelea suala zima la Madiwani. Tunashukuru Madiwani sasa watalipwa kwa kupitia Serikali Kuu, lakini sisi wote tunafahamu, nami nafahamu hata Mheshimiwa Waziri, nawe ni Mbunge, kuna Madiwani kule Jimboni kwako. Hawa Madiwani wote wanafanya kazi kubwa sana katika kuwahudumia wananchi. Hii posho inayolipwa, bado ni ndogo sana. Napendekeza kwamba kuwe na nyongeza pia ya posho yao licha ya kulipwa kutoka Serikali Kuu. Ikiongezwa tutawasaidia sana ili waweze kufanya kazi vizuri na kutimiza majukumu yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee hapo hapo, hizi Halmashauri zilikuwa zinalipa hii posho, tumewapa hiyo nafuu. Hii hela ambayo tumeiokoa ningependekeza yatolewe maelekezo maalum ielekezwe kwenye nini? Nafahamu kwenye Jimbo langu kwa mfano itaokolewa karibu shilingi milioni 10 kwa mwezi au zaidi. Hii fedha inatosha darasa moja la Shule ya Msingi, inatosha kupaua majengo yale ambayo ni maboma. Tusipotoa maelekezo maalum au wasipokuja na mpango maalum wa kuzitumia zile fedha ambazo tumeziokoa kwa Serikali Kuu kulipa, matumizi haya hayataeleweka na huku kuokoa hakutakuwa na tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza TAMISEMI itoe maelekezo maalum kwa fedha zilizookolewa kutokana na Serikari Kuu kulipa posho za Madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda sasa kuzungumzia misamaha ya kodi kwa taasisi za dini. Ninakushukuru kwanza Mheshimiwa Waziri pamoja na Serikali mmekuja na msamaha mzuri. Napenda nikwambie kwamba kuna kigezo kilichowekwa cha kusema kuwe na mkataba kati ya Serikali na mtoaji msaada ndipo msahama utolewe. Kuna taasisi ndogo nyingi za dini ambazo zinatoa misaada na nitakupa mfano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwenye Jimbo langu Kilolo kuna container lenye dawa, lenye vitanda kwa ajili ya Hospitali ya Wilaya ya Kilolo, lina miaka mitatu pale bandarini na lilitolewa na Kanisa na suala ilikuwa ni msahama ambao ulichukua zaidi ya miaka miwili kupatikana. Sasa hivi tunashughulikia storage na mpaka sasa sijui itatolewa lini? Ni kwa sababu ile ni taasisi ndogo, lakini imetoa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatutaweza pengine kufanikiwa kuingia mikataba na taasisi zote, lakini zile taasisi ambazo zimesajiliwa na tunajua zinatoa msaada, tukisema kwamba lazima tuingie mikataba, tutachelewa. Hapa sisi wote kwenye maeneo yetu tuna taasisi za dini ambazo zinasaidia na mara nyingi zinakwama kwenye misamaha na wakati huo huo zinachelewesha na kama nilivyozungumza hapa, lile ni kontena la dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua kuna nchi hapa kuna kontena lilipuka na moto ukaunguza nusu ya mji, lakini tumeacha kontena lenye dawa ambazo najua zime-expire lipo bandarini na halijapatiwa msamaha hadi leo. Sasa ni storage, wakati huo huo tunajua lina viashiria vya hatari kwa sababu hatujui zile dawa ziki-expire zitafanya nini? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimetoa huo mfano ili kuona umuhimu wa kuharakisha misamaha hasa tunapopokea misaada ambayo tunaihitaji. Kwa sababu sasa pale Kilolo vitanda na dawa tunanunua, Serikali inatoa hela. Kama tungepokea vile, tungekuwa tumeokoa hela nyingi sana. (Makofi)

Mheshimiwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa kwa mchango mzuri sana.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, nashukuru. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kuridhia Itifaki ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia Itifaki hii ya Jumuiya ya Afrika Mashariki ya Viwango vya Afya ya Mimea, Wanyama na Usalama wa Chakula. Kwanza kabla ya kuendelea naunga mkono hoja na nafanya hivyo kwa sababu kuna baadhi ya vitu vilivyomo katika Itifaki hii hata kama tulikuwa tunaogopa na hata tungeendelea kuogopa, hatuwezi kuvizuia.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano Article ya nne inazungumzia framework for managing pests na tunafahamu kwamba pests hawana mipaka, hata nadhani mwaka huu kulikuwa na nzige hawawezi kusema hawa wamesaini au hawa hawajasaini, wata-cross na kama hakuna hiyo management maana yake ni kwamba tutakuwa hatufanyi jambo lolote la maana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kuna mambo ya cross pollination ambalo hilo ni la kuliangalia, kwa mfano hata tunapozungumzia kwamba hatutaki GMO, lakini kuna nchi ambazo tunapakana na wanalima na wanaweza wakawa wanakubali GMO, sasa cross pollination pia hatuwezi kuzuia nyuki kuvuka mpaka kwa mfano. Kwa hiyo kuna vitu ambavyo hata kama hatutaki kwa sababu tunapakana na nchi na hatujajenga ukuta au kuzuia kwa namna yoyote ni lazima vile vitu tutavipata tu. Kwa hiyo kwa kusaini hii Itifaki inatoa room ya discussion ambayo inaweza ikasababisha hayo mambo tukaya-manage vizuri zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ili tuweze kunufaika sasa na Itifaki hii ambapo ni kweli kwamba sisi ni wazalishaji wa chakula na sisi tunaotoka kwenye maeneo tunayozalisha chakula kingi kama mahindi na hata sasa hivi wanazungumzia parachichi, kuna mambo ambayo ili tuweze kunufaika ni vizuri Serikali yetu ikajiandaa. Jambo la kwanza ni maabara na vifaa vya kupimia ubora wa hayo mazao kutoka kwenye chanzo chenyewe. Kwa mfano, mtu anaposafirisha mahindi kutoka Iringa, Sumbawanga au Mbeya halafu afike mpakani ndipo aambiwe hayana ubora wa kutosha, itakuwa ni changamoto na inaweza ikawa ni disaster kubwa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hivyo wakati tunapokwenda kusaini hii Itifaki, basi zile sehemu zinazohitaji maabara ya kupimia haya mazao ziwe zimeandaliwa ili wakulima waweze kunufaika. Kwa hiyo, maabara kama hizo na hata sasa hivi kwenye kilimo hiki cha parachichi zile maabara za kupima ubora ambapo sasa mtu anapokuwa na hiyo certificate tangu kwenye chanzo, kwa sababu mara nyingi processing za certificate zinaweza zikafanyiwa mahali ambapo sio kwenye chanzo cha hayo mazao. Kwa hiyo certification ikifanyika kule itakuwa rahisi zaidi kwenye kuhakikisha kwamba tunanufaika na protocol hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haiishi tu kwenye maabara zenyewe, bali pia kuwajengea uwezo wakulima kuelewa viwango, kwa sababu wafanyabiashara wapo lakini wengi hawaelewi hivi viwango. Nilifanya utafiti kidogo, kwa mfano, maandalizi yapo ya kutosha sana kwenye sekta ya chakula TBS imesha-harmonize karibu kila kitu kwenye East Africa, kama ni vyakula vilivyobaki basi ni vichache sana. Hata hivyo, pamoja na hiyo harmonization ambayo imeshafanyika, ni wakulima au wafanyabiashara wangapi wanajua au labda kuna haja ya kutengeneza manual ya standards hasa kwa vile vyakula ambavyo tuna-export sana na zikawepo kwenye sehemu ambazo watu wanaweza kuzi-access, tena zikatengenezwa kwa lugha rahisi ili kila mtu aweze kuelewa standard zetu ni zipi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nazungumza hivi kwa sababu, kwa mfano TBS waki-harmonize na ziko pale TBS kwenyewe na wakulima hawaelewi, bado watataka ku- export kitu ambacho kinaweza kisiwe competitive au kikawa haki-fit kwenye hii protocol. Hiyo inaweza ikawa ni changamoto ambayo inaweza ikasababisha hii protocol ikatupa disadvantage badala ya advantage kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hilo napenda pia liangaliwe kwamba kuna elimu kiasi gani ili tuweze kunufaika? Maana yake hofu hii inaweza ikawa hatukujiandaa, sasa tumejiandaa: Je, wananchi wa kule Iringa, Mbeya na Sumbawanga, wanaelewa maandalizi tuliyoyafanya ili waweze ku-export? Kwa sababu kweli sisi ni beneficiary wakubwa sana wa hii, lakini kama kutakuwa na maandalizi ya kutosha.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa kwa kweli ni vizuri sana kuiomba hata Serikali kuangalia, kwa sababu kama tunaendelea kuzungumza kwamba kilimo ni uti wa mgongo na ufugaji ni uti wa mgongo pia, lakini kama tusipotengeneza mazingira ya ku-export tukabakia kula wenyewe, maana yake ni kwamba haitawezekana kuweza kunufaika na baadhi ya protocol ambazo zinatufanya tuweze kufaidika zaidi. Hiyo hofu inaweza ikawa ilikuwa inatokana tu na kutokuelimisha watu ambao wanaweza wakafanya biashara vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitu kingine ambacho ningependa tu kukizungumzia cha mwisho ni huu urahisi wa hizi certification wakati wa kusafirisha haya mazao. Kwa sababu inazungumzia, wakati unapotaka kusafirisha upate wapi vibali vya kusafirishia. Sasa kuna mlolongo wa vibali kwenye nchi mbalimbali, hata kwenye nchi yetu unakuta kunakuwa na mlolongo wa vibali vingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, ni lazima tuweke one stop center ya certification ili mtu anapokwenda awe na one stop center ya certification. Anataka ku-export, haya hiyo Phytosanitary Certificate aipate pale pale ambapo ambapo anapata kibali cha ku-export, aipate pale pale ambapo anapatia leseni, hizi tunazozungumza hizi center ambazo ni sehemu moja na hizi za Phytosanitary ziwepo hapo ambapo tayari tumeshaanza kurahisisha. Isije ikawa tunatengeneza hii kikawa kikwazo sasa; mtu amefika kwenye One Stop Center anapata vibali vyote, anaambiwa sasa Phytosanitary huna, Sanitary Certificate huna, hiyo katafute Wizara ya Kilimo.

Kwa hiyo, ku-merge kwa sababu hiki ni kitu kipya, kuna importance ya ku-merge hiyo ili ije isababishe sasa ule urahisi uwepo. Pale palipowekwa zile One Stop Center; TRA, sijui nani, wote wale, naye awepo. Kama kuna haja ya kuangalia document mahali, iwe rahisi zaidi ili hii isije ikazalishwa kuwa barrier. Tusaini halafu baadaye iwe barrier wakati wa implementation.

Mheshimiwa Naibu Spika, yangu yalikuwa ni hayo. Nashukuru sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa ili niweze kuchangia. Nianze kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa fedha za madarasa, tumejenga madarasa 73 ya sekondari kule Kilolo, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa na mambo machache ya kuchangia kwa haraka kulingana na muda. Kwanza ni suala la Aids Trust Fund, Mfuko ulioko chini ta TACAIDS pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mifuko mingi tunayoianzisha hapa Bungeni huwa ina chanzo mahsusi cha mapato, lakini Mfuko huu ulianzishwa kwa kutegemea kwanza baeti ya Serikali, imetengwa shilingi bilioni moja na ndiyo inayotengwa kila mwaka, harambee pamoja na michango mbalimbali inayotokana na wahisani mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, kama ilivyo katika Mifuko mingine, uwe Mfuko wa Maji, Barabara na Mifuko mingine mbalimbali, Mfuko huu pia utafutiwe chanzo mahsusi kutokana na tozo au da mbalimbali mahali fulani ambazo tayari zipo ili uweze kuwa stable zaidi. Kwa sababu tunazungumzia jambo ambalo bado mpaka sasa kuna watu 200 wanaambukizwa UKIMWI kila siku, ambayo ni 73,000 kwa mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii bado ni idadi kubwa, lakini hatuko sustainable. Zaidi ya 90% ya bajeti inatokana na misaada na kama ikitokea siku moja wafadhili tukatikisika kidogo tu, hatuna uwezo wa hata 5% wa kuweza kujifadhili. Kwa hiyo, huu mfuko lengo lake tungeujenga taratibu ili wafadhili watakapokuja kutikisika kidogo, basi angalau tuwe stable tuweze kununua angalau paracetamol kwa muda kadhaa wakati tunaendelea kujipanga.

MHE. ENG. STELLA I. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mtoa taarifa, Mheshimiwa Engineer Stella Manyanya.

T A A R I F A

MHE. ENG. STELLA I. MANYANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Naomba pia nimpe taarifa Mheshimiwa anayechangia kwamba ni kweli kabisa naungana naye katika kuongeza fedha kwenye mfuko huu, kwa sababu katika eneo la kutoa elimu, tuko nyumba sana. Kwa mfano, sasa hivi kuna hatari kubwa inayoendelea kwamba hizo condom tunazosisitiza kwamba watu wawe wanazitumia, kwenye maeneo ya vijijini na siyo vijijini tu, hata mjini, lakini hasa suala hili nimeliona vijijini, unakuta watoto wanachukua hizo condom ndiyo wanageuza kuwa mipira na unakuta mtoto analia kabisa naomba condom yangu, condom yangu, kumbe ameiokota tu kwenye majalala huko. Kwa hiyo, bado inahitajika elimu ya kutosha na iwafikie wananchi wote. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Nyamoga, unapokea taarifa?

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeipokea taarifa hiyo. Sasa naomba kuchangia pia kuhusu magonjwa yasiyo ya kuambukiza, lakini mimi nitachangia kipengele kimoja kuhusu suala la wataalam wa mazoezi (physiotherapists). Wizara ya Afya inafahamu kwamba chuo kinachotoa taaluma hiyo kwa sasa ni kimoja tu cha KCMC; na hivi tunavyozungumza, tuna Physiotherapist 500 tu ambao wana practice nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kawaida, magonjwa kama kisukari, pressure na hayo mengine yanahitaji mazoezi. Hizi Idara kwa sasa hivi, nyingi ziko kwenye ngazi ya Mkoa tu, lakini sasa siyo kama zamani. Zamani vijijini tulikuwa tunapelekewa tu dawa za matumbo, kikohozi na kadhalika; lakini kwa jinsi magonjwa yasiyo ya kuambukizwa yanavyoendelea, hali inahitaji Physiotherapist hadi kwenye Hospitali za Wilaya; na hizi Idara hazipo kwenye Hospitali za Wilaya na ni Idara muhimu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza kwamba Wizara ya Afya iangalie kuongeza vyuo vinavyotoa taaluma ya Physiotherapist, yaani wale watu wa mazoezi. Pia katika ikama, wakati wa ujenzi wa hospitali za Wilaya na hata vituo vya afya, tuangalie uwezekanao wa kuweka hizo ili kuweza kuendana sasa na kasi ya maradhi yasiyo ya kuambukiza, yanayohitaji sana hii huduma ya Physiotherapist. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ninalotaka kuzungumza ni kuhusu bajeti ya maendeleo kwa Tume ya Dawa za Kulevya. Kwasababu tuna chaguzi mbili; au tuwe na watu wengi sana humu ndani (hapa nchini) wanaotumia madawa ya kulevya, au tuzuie yasiingie kwa kiwango kikubwa. Kuzuia ni kwa kununua mitambo kwenye maeneo mbalimbali na mitambo hiyo inahitaji bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza bajeti hii iangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutulinda na kupata nafasi ya kuchangia kwa maandishi. Hii ni kwa sababu sikuweza kupata nafasi ya kuchangia kwa njia ya hotuba Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza Wizara iangalie na kukiondoa Kijiji cha Kilolo ambacho ndipo makao makuu ya Wilaya yalipo. Hiki ni kijiji na si mji na kina hati ya Kijiji, kina Serikali ya kijiji na kina vitongoji; kwa hiyo siyo sawa wao kuwekwa kwenye orodha ya miji na kulipa zaidi ya shilingi 27,000. Ifahamike kwamba vipo vijiji vyenye hali bora zaidi kuliko Kilolo na vinalipa shilingi 27,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu umuhimu wa kutengeneza kanuni na taratibu za kusajili vituo vya vijijini; hii itapunguza gharama za mafuta na kufanya biashara halali kuliko sasa ambapo biashara haramu na hatari inaendelea.

Kuhusu Bwawa la Mwalimu Nyerere naiomba Serikali kuweka mkazo katika ujenzi wa bwawa hili na kuondoa vikwazo vyote vinavyochelewesha ujenzi huo.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafsi ili na mimi niweze kuchangia mapendekezo ya mpango. Nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutekeleza miradi mbalimbali kwenye majimbo yetu ikiwemo jimbo la Kilolo. Pia niishukuru Serikali kwa wasilisho la mpango ambao mmeuwasilisha. Huu ni wakati wetu ili sisi tuweze kutoa maoni na mapendekezo ambayo yatasaidia katika kuboresha mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nianze kwa kuzungumzia mashirika ya umma na namna ambavyo yanafanya kazi zake na jinsi ambavyo tunaweza tuyakaboresha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii ina zaidi ya mashirika ya umma 200, sina idadi yake kamili, lakini sina hakika kama mashirika haya yote yana ufanisi na tija ambazo tunazihitaji. Ninaona kwamba kuna haja huu mpango wa Serikali ukaja na tathimini ya mashirika ya umma ili kujua kama yote yanahitajika na kama kweli yote hayafanyi vitu vinavyojirudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano; nimesoma kwenye taarifa nikaona kuna mashirkia mawili na nikaangalia kazi yalizozifanya kwa mwaka uliopita. Shirika la kwanza linaitwa CAMARTEC. Kwenye taarifa yake wametaja vitu walivyovifanya mwaka jana. Kwanza, wametengeneza tella moja, lKINI sijajua ni tella la nini? Pili, wametengeneza mashine mbili za kubangua korosho, kingine walichotengeneza ni mikokoteni 10 ya kuvutwa na Wanyama, pia wametengeneza mashine nne za kupura mtama. Naomba niishie hapo, na kuna vingine pia wamefanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mawazo yangu nafikiria, hivi vitu ndivyo vinavyoweza kufanywa na SIDO na Mashirika mengine. Sijajua kama hii ni taasisi ya ubunifu au ni taasisi ya uzalishaji? Kama ingekuwa ni ya ubunifu mashine moja ya kupura mtama ingetosha ku-display ili wengine nao watengeneze. Pia kama ni ya uzalishaji kwa nini wazalishe nne? Kwa hiyo kwa kifupi ni kwamba zipo baadhi ya taasisi hazihitajiki au kama zinahitajika kuna namna ya kujirudia katika utekelezaji wake. Kwa hiyo ni muhimu kufanyia tathimini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikaenda kwenye shirika lingine la umma linaitwa TEMDO, nikasoma. Kitu kilichofanyika ni kukamilisha kwa majokofu mawili ya kuhifadhia maiti. Sasa haisemwi baada ya hayo majokofu mawili tunafanyaje labda ni kwa ajili ya kuwaonesha wengine ili watengeneze mengi au hayo hayo ndiyo wameyauza au ni kitu gani kimefanyika? Sasa tukienda hivi maana yake ni kwamba tuna allocate fedha kwenye makampuni ambayo tija yake ni ndogo halafu hatu-allocate fedha kwenye sehemu ambazo tija ni kubwa na matokeo yake ni kwamba kuna upotevu wa rasilimali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kule kuna taasisi hizo zina wafanyakazi, zina namna nyingi, tahthimini ingeweza kusaidia kuona umuhimu wa kuendelea kuwepo au kutokuwepo. Hivyo basi mimi nafikiri ni muhimu sana hilo tukaliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunazungumza hivyo, kuna shirika hili la Kibaha, hiki kiwanda cha viuadudu ambacho tumekuwa tukikizungumzia hapa kila wakati, kimekwishatumia shilingi bilioni 83 na bado hakifanyi kazi. Sasa kama tungekuwa tayari tumesha-restructure hizi kampuni zikawa chche maana yake tungeweza kuwa na rasilimali nyingi kuwekeza kwenye hii ya viuadudu ambayo sote tunajua kwamba ingeweza kuokoa fedha nyingi kutokana na uwekezaji ambao tungeweza kuufanya kwenye dawa za kuulia wadudu. Hata changamoto ya Malaria ingeweza kupungua na zile fedha ambazo tunatumia kwenye mambo ya malaria zingeweza kuokolewa. Kwa hiyo ningependekeza kwamba, hizi kampuni zaidi ya 200, Serikali kwenye mpango wake iyafanyie tathimini ione kama zote zina tija. Kama kuna ambazo hazina tija ziondolewe ili tusiendelee kuwekeza kwenye sehemu ambayo hakuna tija yoyote katika kuwekeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii mifano miwili inaweza ikatoa picha halisi ya mengine mengi ambayo unaweza ukakuta kile kinachofanyika hakiwezi kuwa na tija. Huwezi ukawa na tija ya tella moja, huwezi ukawa na tija ya mkokoteni ambao hata watu wengine huko wanatengeneza. Hatuhitaji kampuni ya kiserikali kuanza kutengeneza mikokoteni ya kuvutwa na ng’ombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niizungumzie pia benki ya kilimo (TADB). Kwanza niipongeze Serikali imewekeza shilingi bilioni 60 ni jambo zuri. Pia mtaji wake sasa umekwishafikia shilingi bilioni 268, ni hatua kubwa. Hata hivyo hii benki ni invisible, haionekani. Hata hapa Dodoma nikiwauliza Waheshimiwa Wabunge hii benki iko wapi hata hapa Dodoma Makao Makuu Hawajui. Mimi nilifanya kazi ya kuitafuta, iko nane nane ndani kwenye fence. Sasa benki zote ziko hapa mjinii, hii iko nane nane tena kwenye fence na wakati huo wakulima wako vijijini. Tufanye tathimini ya hii benki ili kila mkulima aweze kuielewa vizuri hii benki na aweze kuelewa namna anavyoweza kui-access ili wakati tunapokuwa tunafanya block farming ziweze kuunganishwa na hii benki ili uwekezaji huo uweze kuwa na tija. Nani atajua kuna benki ya kilimo iko pale nane nane ilhali hata kibao hakipo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kwenye mikoa yetu tunayotoka, wengi wetu hapa tumesema, mimi Iringa sijaiona, wala Kilolo sijawahi kuiona na kama Mimi Mbunge mwenyewe sijawahi kuiona na hata wakulima wenyewe pia hawajawahi kuiona na hawaielewi. Kwa hiyo, kwa sababu ndiyo benki pekee inayowekeza kwenye kilimo, ukisema benki sio mfuko. Mfuko unaweza ukawa na ofisi mahali lakini benki sisi Watanzania tunaelewa benki utaiona popote pale. Sasa benki gani haionekani? Hii ni changamoto, ipo ina mtaji basi sasa ionekane ili wananchi waweze kufanya uwekezaji. Hilo litakuwa ni jambo la muhimu sana kwa sababu linaweza kusaidia katika kuboresha kilimo katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie jambo la mwisho katika mchango wangu ambalo linahusu mradi wa Bwawa la Mwalimu Nyerere. Kwanza nipongeze kwa hatua iliyofikiwa. na mimi ninahakika kwamba mradi huu utafanya kazi vizuri tu. Lakini, ili mradi ule uweze kufanya kazi, raw material yake ni maji na haya maji yanatoka kwenye vyanzo na Kilolo ni mojawapo ya vyanzo. Sasa kama wewe unajenga Bwawa lakini huwekezi kwenye kulinda vyanzo vya maji au kuwa na miradi itakayovifanya vyanzo hivyo vya maji viendelee kuwa endelevu maana yake ni kwamba raw material rasilimali ya ule mradi haipo. Sisi tunajua sasa hivi kwa mfano kilimo cha miti kinatakiwa kiwe na tija, sasa kama hakutawekwa ruzuku kwenye kilimo cha miti ili wakulima wa miti kwenye milima ya udzungwa waendelee kulima miti, mti mmoja uuzwe shilingi 2000 wataikata, watalima mazao mengine na hayo maji hayatakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa wakati huu tunapozungumzia mabadiliko ya tabia ya nchi ni ushauri wangu kwa Serikali, maeneo yote yenye vyanzo vya maji yanayolisha Bwawa la Mtera, Bwawa la Mwalimu Nyerere, Bwawa la Kidatu na Mahali mengine ikiwemo maeneo kama Kilolo, Makete na maeneo mengine yafanyiwe tathimini ya kupewa ruzuku kwenye kilimo cha miti kitakacholinda vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia hoja hii muhimu ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. Kwanza nitoe shukrani zangu za dhati kwa Wizara hii lakini pia kwa Mheshimiwa Rais kwamba baadhi ya mambo tuliyoyaomba mwaka jana kwa upande wa Jimbo langu yameanza kutekelezwa, hasa ujenzi wa Ofisi ya TAKUKURU ambao walikuwa wanakaa kwenye godauni, sasa umeanza tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo napenda kushukuru, ni kwamba tumeshawasilisha sasa ombi letu la ukarabati wa zahanati kupitia Mfuko wa TASAF. Zahanati ya Kijiji cha Mkalanga na Zahanati ya Kijiji cha Winome ambazo wananchi ndio wameibua miradi hii ili zile ziweze kukarabatiwa na kukamilika kupitia Mfuko wa TASAF. Naomba kupitia kiti chako basi Wizara hii iweze kuzifanyia kazi angalau kwenye bajeti hii ili zahanati hizi mbili ziweze kukarabatiwa na kwa umahiri wa Mawaziri pamoja na Watendaji wa Wizara hii, nina hakika ombi hili litapokelewa kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuzungumzia mambo machache, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Utawala na Serikali za Mitaa, kwa hiyo, mambo mengi kwa kweli tumekuwa tukishauri kwenye Kamati. Jambo la kwanza ambalo tumekuwa tukiendelea kushauri, nami ningependa kulisisitiza hapa ni kuhusu watumishi wanaojitolea kwenye sehemu mbalimbali. Watumishi hawa wanajitolea kwa muda mrefu, wengine miaka sita wengine nane wengine saba, hasa walimu na wale wa kwenye sekta ya afya, na wengine wanajitolea kwenye mazingira magumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hakuna mfumo maalum wa kujitolea, japo mahitaji ya kujitolea yapo, tulitoa ushauri utengenezwe mfumo maalum unaowatambua watu wanaojitolea ili inapofika wakati wa kuajiri tuwe na hiyo database. Kwa sababu, siku hizi mtu anakwenda tu anaongea na Mkuu wa Shule na anaanza kujitolea, au anaenda Zahanati, anaanza kujitolea. Hii haitoi fursa sawa. Kwa sababu, mtoto wa masikini anaweza akaenda pale akakataliwa, lakini mtoto wa Mtendaji wa Kata au Mwenyekiti wa Kijiji, akapata fursa kwa mamlaka au mtoto wa mtu mwingine mwenye mamlaka. Kukiwa na mfumo mzuri wa kujitolea ambapo tunajua mahitaji yapo, utasaidia kufanya acceleration wakati wa kuajiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba hii haipo, naomba iangaliwe namna itakayokuwa fair, ya kuwafanya wale waliojitolea muda mrefu kwenye hizi ajira waweze kupata kipaumbele. Jambo la pili ambalo ningependa kulisema na tumelizungumza pia hata kwenye Kamati, ni suala zima la mafunzo. Utakuta kwenye maeneo mengi wanaohudhuria mafunzo ni viongozi katika ngazi za Wilaya, labda wakuu wa Idara na wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao Watendaji wa Kata, na kwa mujibu wa taratibu na Kanuni za muundo, wao ndio kama viongozi katika Kata; na wale watendaji wengine awe Afisa Kilimo au Afisa Mifugo, wanaripoti kwao. Jambo la kwanza, pamoja na kwamba vitendea kazi hawapewi, unakuta wa Mifugo wamewapa, labda wa elimu wamepewa pikipiki, yeye bosi wao hana hata baiskeli. Hilo linaweza likawa linaangukia TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye mafunzo sasa. Tulishauri na ninaendelea kushauri kwamba mtu hawezi kutoka Chuoni au huko aliko akaanza kufanya kazi zile bila kupata mafunzo maalum. Tulishauri Chuo cha Utumishi wa Umma kiweze kutoa hayo mafunzo ili watumishi hawa wa ngazi ya Kata na hatimaye wa ngazi za Vijiji waweze kuwa na umahiri wa kutenda kazi zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa Watendaji wa Kata kwa kuwa tumesema ni Wakurugenzi katika ngazi ya Kata, waweze kujua wajibu wao wa Ukurugenzi katika ngazi ya Kata; wanawajibika kufanya nini? Kwa sababu, wakati huo utakuta kwenye Halmashauri kuna Masijala na nini; nenda kwenye ngazi ya Kata, hata Folio kwenye file, huyu mtu hajawahi kufundisha na haelewi. Kwa hiyo, haya ni mambo ya muhimu sana ambayo tungependa yatiliwe mkazo kwenye bajeti, hasa kwa ajili ya Chuo cha Utumishi wa Umma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo naomba, hili ni wasilisho la ombi langu ni kuhusu Watumishi Housing. Sasa hivi ujenzi wa nyumba nyingi unaendelea mijini. Nitaje mfano kama Kilolo; Mji wa Kilolo ni Mji unaokua. Watumishi wengi pale kila siku tunafukuzana nao kwa sababu wanataka kuishi Iringa Mjini na ukiangalia ni kwa sababu pale Kilolo hakuna nyumba hata za kuweza wao kupanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napendekeza, hizi Wilaya ambazo zimejengwa kwenye maeneo ambayo hayakuwa Miji, zipewe kipaumbele kwa kujengewa nyumba na Watumishi Housing ili miji ile kwanza iweze kukua, na pia kuleta tija kwamba watumishi watakaa pale, kwa sababu, vinginevyo utakuwa unawabana watumishi kukaa kwenye sehemu ile, lakini sasa hakuna makazi ambayo wanaweza kukaa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Watumishi Housing i-plan vizuri ili tuweze kuwa na makazi ya kutosha hasa kwenye eneo hilo nililolitaja la pale Wilaya ya Kilolo ambapo Mji ule ni mdogo na unahitaji sana huduma hiyo. Jambo la mwisho ambalo ningependa kuchangia ni kuhusu upungufu wa watumishi. Wilaya ya Kilolo kama zilivyo Wilaya nyingi za vijijini ina upungufu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeweza kusoma takwimu nyingi, lakini kwa sababu ya muda niongelee kwenye sekta ya afya. Ili angalau tuweze ku-operate, Zahanati ambazo zimemalizika kujengwa na Vituo vya Afya tulivyomaliza kujenga, tunahitaji watumishi 39. Kwa hiyo, nikitaja yale maelfu, najua huenda yasiwe na tija sana. Hawa 39 watatusaidia angalau kwa kuanzia na hawa wanaweza kupelekwa kwenye Vituo ambavyo, ni kama Zahanati ambazo hazijaanza kabisa kama Zahanati ya Mbawi, Masege, Lugalo, Ilole, Mlafu, Ibofwe, Ikuka na Idunda Vituo vya Afya vya Ng’uluwe na Nyalumbu ambavyo hivyo nilivyovitaja, vimekamilika, lakini sasa hatuwezi kuanza kufanya chochote kwa sababu hakuna watumishi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ni kwa sababu najua kuna ajira hivi karibuni, basi ninaomba kwamba yale maombi yetu yatakapoletwa ieleweke kwamba hizi ninazozitaja zinahitaji kwa kiwango kikubwa sana attention ya karibu na kama…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nishukuru sana kwa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii muhimu ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza mimi nitoe shukrani zangu za dhati kwa Serikali ya Awamu ya Sita, Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waziri na Naibu Waziri, Katibu Mkuu pamoja na Watendaji wa Mkoa. Vilevile Injinia Joyce Bahati wa RUWASA lakini pia ndugu yangu Palanjo wa IRUWASA kwa kazi kubwa inayofanyika katika Jimbo la Kilolo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliposimama hapa mara ya kwanza kuchangia Wizara hii kuna mambo kadhaa niliomba mwaka jana, na niishukuru sana Wizara hii kwa usikivu. Niliomba usambazaji wa maji katika Mji wa Ilula. Ninashukuru sana Wizara hii imechukua hatua, milioni 500 zilizotolewa kwa ajili ya miradi ya UVIKO zilipelekwa pale na usambazaji umefanyika. Ninawaomba wale wanahabari waliokuwa wanataja Vitongoji vya kuzunguka Ilula havina maji waende sasa wakapige picha kwa sababu maji yanatoka ili tujue walikuwa na nia njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi tu, wiki iliyopita Mheshimiwa Waziri kwa usikivu wako umeongeza shilingi milioni 500 kwa ajili ya Mji wa Ilula. Ninakushukuru sana, tenda ile itangazwe mapema ili ule usambazaji uendelee katika vitongoji vyote vya Kata ya Ilula na Nyarumbu ili wananchi wale waendelee kunufaika na maji. Haikutosha kupitia IRUWASA shilingi milioni 350 kwa ajili ya Mji Mdogo wa Kilolo ambazo pia juzi kwenye mazungumzo umepitisha. Kwa maana hiyo ndani ya bajeti ya mwaka huu tayari tuna shilingi milioni 850 zinaenda ambazo zimeongezeka katika Bajeti iliyopita. Ninakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikakushukuru kwa ajili ya miradi mingine niliyoomba mwaka jana Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri mmeifanyia kazi. Mradi wa Uhambingeto ambao umekuwa ni chechefu kwa muda mrefu. Mradi huu tayari umeshatafutiwa mkandarasi na amepatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoomba kuweka sign ile mikataba mapema ili mradi ule wa Kata ya Uhambingeto uweze kufanyika mapema. Ninashukuru pia kwamba kuna miradi mingine miwili ambayo imechukua muda kidogo kupata wakandarasi lakini tayari imepatiwa fedha. Mradi wa Masege Masalali, Kihesa Mgagao na Mradi wa Ifua – Lisoli ambayo pia tuliiomba mwaka jana na imepata fedha. Mimi ninashukuru sana kwa sababu mmefanyia kazi mapema na ninaona kwamba kuna dalili njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri huwa anasema wali wa kushiba huonekana kwenye sahani na mimi nakubaliana naye. Lakini kuna vijiji na kata ambazo huo wali wa kushiba zinauona ila kama tunavyoenda kwenye hoteli umefunikwa na ile karatasi ya nailoni bado haujafunuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo kata ambazo bado hazijapata maji. Naomba nitaje baadhi ya maeneo. Kata nzima ya Ng’ang’ange haijapata maji tangu kuumbwa kwa ulimwengu. Lakini pamoja na hayo, tunavyo vijiji baadhi ambavyo kuna mradi wa Mto Mtitu ambao ni Mradi wa Mto Mtitu ni mradi wa mkoa siyo mradi wa wilaya. Mradi wa Mto Mtitu maji yake yanapita katika Majimbo ya Kilolo Kalenga, Iringa Mjini pamoja na Jimbo la Isimani. Na huu mradi tayari pendekezo limeshaletwa liko mezani kwako kwa ajili ya kuomba mkopo kwa Serikari ya Korea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba mradi huu ufanyiwe kazi kwa sababu una vijiji vingi sana katika Jimbo la Kilolo pia kikiwepo Kijiji cha Kitoo. Kijiji cha Mtitu chenyewe ambao ndio Mto Mtitu unaitwa nacho bado hakijapata maji na ninaomba mradi huu ufanyiwe design nzuri ili uweze kukidhi pia baadhi ya maeneo ya Kilolo; kwa sababu chanzo ni Kilolo lakini ukiangalia Vijiji vya Kilolo ni vichache vitakavyopata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi wa Kilolo – Isimani ambao Mheshimiwa Waziri unaufahamu, ulishautembelea. Mimi pamoja na Mheshimiwa Lukuvi wa Isimani tunakuomba mradi ule ukamilike. Umefika asilimia 64 na imebaki kidogo, na una-cover vijiji vingi sana vya Kilolo pamoja na vya Isimani. Ninakusihi sana katika bajeti ya mwaka ujao ukamilishe mradi ule ili wananchi wa Kilolo na wananchi wa Isimani waweze kunufaika na mradi ule kwa sababu ni mradi mkubwa ambao una maslahi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nitoe ushauri mdogo kuhusu miradi iliyopo katika Jimbo la Kilolo. Jimbo la Kilolo lina vyanzo vingi vya maji kwa hiyo, miradi mingi ni miradi midogomidogo kwa sababu tukitengeneza miradi mikubwa itakuwa gharama kubwa isiyokuwa na umuhimu. Nimeona kuna tendency ya kuiangalia kwa ukubwa miradi mikubwa lakini hii miradi ya Shilingi Milioni 500 tayari umeshasambaza maji vijiji vitatu, Shilingi milioni 600 umeshasambaza maji kata tatu, kidogo inapewa umuhimu mdogo kutokana na udogo wake kwa sababu ni ya gharama ndogo. Mimi napenda hii miradi ipate kipaumbele imalizwe mapema kwa sababu miradi mikubwa inachukua muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu wa pili unahusu suala la mita za maji. Mheshimiwa Waziri unafahamu kwamba kwenye umeme tumeshatoka kabisa kwenye post paid watu kuzungukazunguka kwenye nyumba kusoma mita ni unnecessary.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani pale Mkoa wa Iringa mmeshajaribu prepaid na inafanya kazi vizuri. Mimi ninaomba twende kwenye prepaid tuachane na watu kuzunguka, mwisho watu watapigwa mawe waambiwe ni panya road kumbe ni wasoma mita. Kwa hiyo, mimi ninaomba sana kwamba twende kwenye prepaid tuachane na haya mambo ya postpaid. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda kushauri ni Jumuiya hizi za Usimamizi wa Maji. Mheshimiwa Waziri anafahamu kwamba miradi hii imekuwa mingi na inakamilishwa kwa haraka, lakini ni kweli kwamba hakuna mfumo bora wa usimamizi wa hii miradi kwenye vijiji na hizi Jumuiya za Usimamizi wa watumiaji maji bado hazijawa imara vya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba kuwe na utaratibu mzuri ili miradi hii iweze kuwa bora na endelevu. Na tukumbuke kwamba kwenye vijiji vyetu si kwamba sasa hivi watu wanataka kuchota maji kwenye vituo tuu. Kama sisi tulivyo mijini na wao pia wanataka maji yafike kwenye nyumba zao. Kwa hiyo, hizi Jumuiya zikiimarishwa zitasaidia kuweka taratibu nzuri za kuingiza maji kwenye nyumba zao. Mimi naomba sana hizi Jumuiya ziangaliwe ili tuweze kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja na nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukue nafasi hii kumshukuru mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi tena ya kuweza kuchangia hoja hii. Nichukue fursa hii pia kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa jinsi ambavyo ameendelea kutekeleza majukumu yake kwenye miradi mbalimbali na wananchi wa Kilolo wamenituma nishukuru sana kwa mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, orodha ni ndefu sitaweza kuimaliza, lakini tushukuru kwamba baada ya miaka 30 ya kusubiri ameweza kutoa fedha kwa ajili ya ufufuaji wa mashamba ya chai ambayo yalikuwa yametelekezwa kwa miaka mingi. Pia zimetolewa fedha za ruzuku ya mbolea na wananchi wa Kilolo wamenufaika sana tunashukuru sana. Pia imetolewa fedha kwa ajili ya ukuzaji wa miche ya parachichi ambayo mkulima alikuwa ananunua kwa shilingi 5,000 na watu wa TARI wametuahidi kuuza kwa shilingi 1,000, ni punguzo kubwa na naamini kwamba wananchi watanufaika, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. Iko miundombinu ya afya, lakini pia iko miundombinu ya elimu, kwa uchache wa muda kwa ujumla wake tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi anayoifanya na nimkaribishe sana Kilolo kwa ahadi yake kwa ajili ya kuja kuhamasisha kilimo cha parachichi, tunamkaribisha sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wananchi wa Kilolo wanamsubiri.

Mheshimiwa Spika, napenda nijielekeze sana kwenye suala la vijana hasa utaratibu wa ajira na kwenye changamoto mbalimbali wanazozipata kwenye masomo. Jambo la kwanza ambalo ningependa kuzungumza ni utaratibu wa ajira kwa vijana wanaojitolea kwenye taasisi mbalimbali hasa kwenye sekta ya elimu na sekta ya afya.

Mheshimiwa Spika, tulishatoa ushauri mara kadhaa tukiwa kwenye Kamati kwamba utengenezwe mfumo maalum wa vijana kujitolea na huo mfumo uanzie jinsi vijana wanavyopatikana. Tukianza kuangalia jinsi vijana wanavyopatikana utengenezwe mfumo ambao hautoi upendeleo. Tukiacha hivi hivi maana yake ni kwamba mtoto wa Mwalimu ndiye atakayejitolea, mtoto wa mkulima hatajitolea na watoto wa watu wengine watajitolea na wengine hawatapata nafasi ya kujitolea. Tuanze na jinsi gani vijana watatakiwa kujitolea.

Mheshimiwa Spika, kitu cha pili, wale vijana wakishajitolea kuwe na mfumo mzuri wa ufuatiliaji ili ule mserereko inapofika wakati wa kuajiriwa waweze kuajiriwa. Sasa hivi hata namna wanavyopatikana wanavyoingia kujitolea bado haiko sawa na Serikali inajua wako vijana wanajitolea, waliingiaje? Ni rahisi kupanga namna wanavyoingia ili kuwafuatilia kwa sababu tukiacha hivi, kwa sababu watu ni wengi hata kuingia kujitolea nayo ni fursa. Kwa hiyo tuangalie namna vijana wanavyoingia kujitolea na jinsi wanavyolelewa mpaka wakati wa kuajiriwa ili uwe mserereko na huo unaweza ukatengenezwa mwongozo ambao Serikali inaweza ikautumia kuhakikisha kwamba kuna utaratibu mzuri hata wa kuingia kwenye kujitolea.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili bado linahusu ajira na jinsi ya upatikanaji. Siku za karibuni kumekuwa na vijana wanaokwenda JKT. Wanapofika JKT unafika wakati wa kwenda kujiunga na jeshi, hizo nafasi zinatolewa pale lakini hakuna uwazi wa jinsi vijana wanavyotolewa JKT na kuingia kwenye ajira. Matokeo yake ni vi-memo vingi vya vijana walioko JKT kwa Wabunge na viongozi tuwasaidie wajiunge na jeshi. Serikali iandae utaratibu mzuri na iweke uwazi kwa vijana wanaokuwa JKT ili wanapoingia jeshini nafasi zinapotolewa kuwe na uwazi ili vijana wale wasiwe wanasema leo wamechukuliwa watatu, ni ndugu pengine wa mtu fulani, kuwe na uwazi wa kueleweka ili Serikali inapowachukua kila mtu aridhike. Wale vijana wanaotoka JKT zile nafasi hazitoshi wale vijana wanaotoka JKT ambao hawakuajiriwa watoke wakiwa wameridhika, lakini kwa utaratibu wa sasa siyo wa wazi, una malalamiko na manung’uniko makubwa na siyo fair kwa vijana kutokujua uwazi huo umefanyika kwa kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado niko kwenye vijana na kwenye sehemu ambazo kidogo zina changamoto. Sijajua kigugumizi cha kuwakopesha vijana wanaosoma vyuo vya kati kinatoka wapi? Vijana hao ni watoto wa maskini, vijana hao wakimaliza vyuo tunawaajiri sasa hivi tuna zahanati, pharmaceutical technician, tuna lab technician wametoka kule. Kwa nini vijana ambao ni wa vyuo vya kati hawapewi mikopo na wakati wa kuajiriwa wanaajiriwa? Wakati wao pia ni watoto wa maskini wakati ada zao nyingine ni ndogo? Tumeongea muda mrefu hapa lakini Serikali haitoi majibu ya kueleweka kuhusu vijana wa vyuo vya kati kupata mikopo?

Mheshimiwa Spika, niiombe sana Serikali na nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunao vijana wengi sana ambao wako vyuo vya kati na wao pia wana haki ya kupata mikopo kama wanavyopata vijana wa vyuo vikuu.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kuhusiana na vijana, ni uunganishaji wa miradi hii inapotengenezwa. Nataka nitoe mfano, hivi karibuni kulitokea tangazo la miradi ya BBT. Naishukuru sana Serikali kwa ubunifu mzuri, lakini kwenye maeneo yetu kuna vikundi vya vijana vya 10% ambavyo vinajihusisha na kilimo. Sasa ilikuwa ni rahisi ku- search vijana ambao tayari wako kwenye kilimo kupitia kwenye mikopo ya 10% na kuwaingiza kwenye BBT badala ya kuchukua vijana wapya ambao watatakiwa kuanza upya na hawa vijana wenye 10% ambao wana mikopo tayari wana mashamba ndiyo maana walikopa na interest yao ni kulima na ndiyo maana wamekopa mikopo ya kilimo. Kwa hiyo kama tungechukua vijana wale maana yake ni kwamba ni rahisi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi naomba BBT itakayofuata tuchukue vijana waliokopa mikopo ya 10%, wafundishwe kwa sababu tayari ni wakulima, wako kwenye kilimo na ndiyo interest yao badala ya kuchukua vijana wapya na hao vijana wa 10% wako waliomaliza vyuo vikuu na wanataka kulima. Kwa hiyo itakuwa rahisi zaidi wao kwenda na kilimo kuliko mpya ambaye ametafuta tu fursa. Napendekeza kwamba hilo liangaliwe ili vijana waendelee kupata mikopo.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa sitendi haki kwa kuwa pia watu wengi wamezoea kuniita mchungaji hapa kama sitazungumzia suala hili la mambo ya mahusiano ya jinsia moja ya ushoga na haya mambo mengine yanayoendelea ya unyanyasaji wa watoto. Pia nitakuwa sijakitendea haki kizazi hiki na kizazi kijacho.

Mheshimiwa Spika, Tanzania hii sisi kama viongozi inabidi tukemee kwa nguvu zote aina yoyote ya unyanyasaji wa kijinsia kwa watoto wetu walioko majumbani na kwenye taasisi. Niipongeze Serikali imepiga marufuku watoto wadogo kwenda shule za bweni, lakini nafikiri kuna hatua zaidi ya kuchukua tena nilikuwa najiuliza ni kigezo gani kilisema la tano ndiyo wanakuwa wameshafikia kwenda boarding? Kwa sababu kwa kawaida kulitakiwa kuwe na kigezo kwamba darasa la tano wana umri gani badala ya kuangalia darasa, tungeangalia umri kwa sababu wengine darasa la tano na bado ni watoto wadogo, lakini kwa ujumla wake ni vizuri tukatengeneza mifumo maalum ya kuwalinda watoto.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine hatuwezi kufundishwa na Taifa lolote jinsi sisi tunavyoweza kukuza mila na tamaduni zetu. Sisi wenyewe tunao uwezo wa kuelewa tunachotaka kukifanya, tunao uwezo wa kuamua namna mahusiano tunaweza kuwa nayo ambayo ndiyo yalijengwa na ndiyo yaliyosababisha sisi tuzaliwe. Kwa kweli tutajenga Taifa zuri kama tutaendelea kuheshimu mila, taratibu na desturi zetu katika mazingira yoyote yale na hapo tutakuwa pia tumelinda imani zetu ambazo sisi sote tunaabudu kwazo na tena kipindi hiki ni miezi mitakatifu kwa kila mmoja. Naomba sana sana kila Mtanzania aone haja ya kuwajibika katika kulinda Taifa letu kwa kutunza mila na desturi zetu.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza na mimi niungane na wabunge wenzangu kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa uwekezaji mkubwa anaoendela kuufanya kwenye sekta ya kilimo. Lakini pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri Pamoja na Katibu Mkuu kwa ushirikiano ambao wananipa mimi pamoja na wananchi wa Kilolo katika miradi mbalimbali. Yapo mambo mengi ambayo tumeshirikiana na Wizara ya kilimo, lakini nishukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa uungwana wake, kwamba ameungana na sisi katika ufufuaji wa zao la chai katika Wilaya ya Kilolo, na kwamba Wizara yake itaenda kuweka historia ya kukuza uzalishaji wa chai kupitia Wilaya ya Kilolo. Napenda kumshukuru sana, kwa sababu hata ninavyozungumza hivi sasa kazi inaendela ya kufyeka mashamba pia na kazi mbalimbali kuhakikisha kwamba Kilolo na yenyewe chai sasa inafufuka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo napenda kushukuru ni uanzishwaji wa kitalu cha miche ya parachichi. Jambo hili nililizungumza kwenye bajeti iliyopita na limefanyika kwa umakini mkubwa. Hivi ninavyozungumza TARI wameanzisha kitalu pale na nina hakika kwamba msimu ujao tutapanda miche kutoka TARI. Ombi langu dogo ni kwamba bei ya miche ile iangaliwe au kama ilivyo kwa mazao mengine wakulima hasa wale walio masikini wapewe miche ile 20 bure watunze vizuri ili waje wavune kwa sababu kuna mazao mengine pia wananchi wanapewa miche bure.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine ambalo ningependa kushukuru ni ile scheme ya Ruaha Mbuyuni, kwamba baada tu ya kupata madhara, majanga ya scheme ile umetusikiliza, umetuma wataalamu kufanya tathmini na hivi tunavyozungumza tathmini imeshafanyika na mimi kwa niaba ya watu wa Kata ya Ruaha Mbuyuni nitoe shukrani za dhati kwa mwitikio wa haraka. Lakini nitoe ombi kata ya Ruaha Mbuyuni Pamoja na Kata ya Mahenge ni kata ambazo ziko maeneo makavu sana. Hivi tunavyozungumza ile sehemu ambayo ilikuwa imwagiliwe kwa scheme ile maana yake mazao yanaendela kuharibika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafahamu kwamba suluhisho la pale ni lazima kuwe na mpango wa muda mrefu; lakini kama kuna uwezekano wa kuwa na mpango mdogo wa muda mfupi wa kuokoa mazao wakati ule mpango wa muda mrefu unaendelea nikuombe sana Mheshimiwa Waziri, pale Ruaha Mbuyuni iangaliwe ili wananchi wasipoteze mazao. Hasara itakayopatikana kutokana na mazao kuharibika kwa scheme ile ni kubwa kuliko fedha tunayoweza kuwekeza ili angalau maji yaende kumwagilia wakati tunaendelea na zoezi la mpango wa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, ninapozungumzia scheme za umwagiliaji, Tarafa ya Mahenge ina scheme tatu lakini zote ziko kwenye hatua mbalimbali hamna iliyokamilika. Scheme ya Mgambalenga ilianza kujengwa miaka mingi kweli wakandarasi wako site lakini haijakamilika. Scheme ya Nyanzwa tuliiomba huu ni mwaka wa tatu iko kwenye usanifu sasa hivi ndio imewekwa kwenye bajeti kwa ajili ya usanifu wa kina. Sasa mimi niombe sana, kwa sababu usanifu ulifanyika kwenye mwaka huu wa bajeti unaoisha kama inawezekana Scheme ya Nyanzwa iwekwe kwenye bajeti ianze kujengwa lakini sasa Scheme ya Ruaha Mbuyuni nayo hii iko kwenye changamoto. Kwa maana hiyo tarafa yote scheme zote hamna inayofanya kazi, na ni sehemu kavu. Kwa hiyo kama tukiacha vile maana yake ni kwamba tutakuwa kwenye changamoto kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana, hasa Scheme ya Ruaha Mbuyuni angalau ifanye kazi wakati tunasubiri hizi nyingine; na hizi nyingine ziangaliwe kwa sababu eneo lile ni kavu na tusipomwagilia maana yake kilimo katika eneo lile hakutakuwa na namna kinaweza kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina jambo moja ambalo ningependa kushauri kuhusu kilimo, hasa kilimo cha mahindi. Kumejitokeza fursa nyingine katika maeneo ambayo tunalima mahindi. Fursa ya wafugaji wakubwa kununua mahindi kwa ajili ya chakula cha mifugo. Sasa changamoto iliyopo ni kwamba wakulima hawa hawakuandaliwa kulima mahindi kwa ajili ya chakula cha mifugo. Walilima mahindi kwa ajili ya chakula chao, inapofika mahindi yamekomaa lakini hayajakauka wale wakulima wanashawishiwa kuuza yale mahindi na bei yake inakuwa kubwa kuliko akivuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutakachokipata ni kwamba hata nyinyi takwimu zenu mnaposema tunatarajia kuvuna mahindi kiasi fulani hamjazingatia hilo kwamba kuna mahindi mengine ni kwa ajili ya mifugo. Sasa tunaweza kuja kupata changamoto ya njaa kwa sababu hii fursa wakulima hawakuandaliwa vizuri kujulishwa kwamba walime mashamba ya chakula lakini pia kuna fursa ya mazao kwa ajili ya chakula cha mifugo na pengine hata aina za mbegu zingekuwa tofauti; mbegu ya chakula cha mifugo na mbegu ya chakula cha binadamu. Mimi hii fursa naiona lakini nadhani Wizara ni vizuri ikaielezea vizuri kwa wakulima ili tusije tukaleta changamoto ya njaa kwa sababu hivi tunavyozungumza ni muda mahindi ni mabichi na uvunaji wa mahindi kwa ajili ya chakula cha mifugo ni mkubwa bila kuzingatia wale wakulima walilima kwa ajili ya nini; na wakati utapofika wa kuvuna tunaweza tukajikuta tunaingia kwenye changamoto ya njaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningependa kuzungumza ni kuhusu udhibiti wa ujazo. Nishukuru kidogo sasa hivi wakala wa mizani wanajitahidi, lakini mara nyingi tumesimama hapa na kuzungumza kuhusu namna gani mazao ya mbogamboga yanavyoteseka kwenye bei, na mazao haya ni yaleyale ambayo yanalimwa, ndiyo ambayo bei zake hazina bei elekezi na wakulima wakati wote wanateseka na ujazo wake haujulikani vizuri. Mazao ya nyanya, viazi, vitunguu, njegere, karoti pilipili hoho, ndiyo mazao ambayo yanalimwa sana kwa mfano kwenye maeneo ya Kilolo; lakini wakati wote wakala wa mizani bado hawajaja na suluhisho la kuhakikisha kwamba sawa wanapambana na lumbesa lakini bei zinabaki zikiwa nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi wamepambana kupunguza ujazo, lakini sasa wakipunguza kunakuwa na bei ya lumbesa na bei ambayo ule ujazo uko flat. Sasa mimi ningeshauri kwamba kuwe na utaratibu mzuri wa kuendelea kudhibiti bei na pia kudhibiti ujazo. Hili linawezekana kama mazao haya yatauzwa kwa kilo. Kwamba kilo moja ni shilingi kadhaa, kilo 10 ni shilingi kadhaa badala ya kuzingatia kifungashio kama ndicho kinachoamua bei ya mazao hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kuhusu miundombinu hasa kwenye miradi ambayo inatekelezwa, na hapa niende moja kwa moja kwenye kushukuru sana hii mradi wa Agri-connect ambao umekuwa ukisaidia sana kutengeneza miundombinu kwenye maeneo ya kilimo, hasa barabara. Na ujenzi huu Mheshimiwa Waziri unajua mara nyingi umekuwa ujenzi wa barabara za lami. Sasa barabara ya lami inaweza ikawa kilomita 18 au 20, lakini barabara za kuingia sasa kwenda ndani kwenye yale mashamba zinabaki zikiwa hazijalimwa. Lakini pia semina na workshops ni nyingi sana kwenye miradi hii. Mimi nikuombe sana, bajeti ziende kwenye ujenzi wa miundombinu na si semina na warsha, kwa sababu Watanzania wameshaelimika, wanataka miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana na naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii na mimi nianze kwa kuishukuru sana Wizara hii ya Kilimo kwa mambo kadhaa ambayo yanaendelea kufanyika pia ninaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita kwa nia na dhamira ya dhati ya kuimarisha kilimo tunaiona kwenye bajeti hii na ninaamini tutaona makubwa katika kipindi hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani zangu nazielekeza kwa Waziri na Wizara nzima kwa jinsi wanavyoshughulikia suala la chai la Kilolo na ninawataarifu tu wananchi wa Kilolo kupitia Bunge lako kwamba muda siyo mrefu suala la Chai Kilolo litakamilika kwa jinsi ambavyo Wizara hii inalishughulikia na nina imani tutakamilisha suala hilo kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili niendelee kushukuru sana Wizara hii kwa jinsi inavyoshughulikia suala la kilimo cha parachichi na uanzishwaji wa kitalu cha miche ya parachichi katika Wilaya ya Kilolo. Hapa nimtaje Dkt. Mkamilo wa TARI ambaye amefika kule na tayari kitalu kile kimeshaanzishwa na tunatarajia kupata miche ya kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapokuwa hapa kwenye eneo la parachichi watu wa Kilolo tumejipanga na tunajua sasa Kilimo kinaendelea lakini changamoto ndogo tuliyonayo wanaolima sasa hivi siyo wananchi wakawaida wengi wanaolima ni wakulima wenye mashamba makubwa kidogo. Sasa hapa ninapendekezo la block farming kwa wakulima wadogo nitakuomba sana Mheshimiwa Waziri upokee pendekezo hili la Vijiji 25 ambavyo wakulima wadogo wadogo wataanza kulima eka moja moja na sisi tutafuta namna nzuri ni eka moja hadi tano lakini tutafuta namna nzuri ya wakulima hawa kuweza kupata farm input lakini kila block itakuwa na zaidi ya eka 50 mpaka 100 kwenye shamba moja. Kwa hiyo, tunalo hili pendekezo tutakukabidhi Vijiji 25 tuanze navyo kwa ajili ya wakulima wadogo wadogo wa parachichi ili tusiwaache nyuma wananchi wa Kilolo halafu wawekezaji wengine wakaja wao wakabaki vibarua. Nitaomba nikukabidhi kwa ajili ya kulifanyia kazi na wewe nitakuomba unipe Afisa ambaye nitakuwa nafuatana naye ili hili liweze kutekelezeka na unaijua ufuatiliaji wangu na hili nalo nitakusumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakuomba pia Mheshimiwa Waziri kuhusu skimu chache ambazo zimetajwa kwenye bajeti ya mwaka jana, skimu ya Mgambalenga imetengewa shilingi bilioni moja lakini mpaka leo kwenye Tume ya Umwagiliaji ukiangalia kwenye randama ukurasa wa 52 utaikuta, bilioni moja ilitengwa na mpaka leo haijatolewa hata shilingi, ninakuomba kwa kipindi hiki kilichobaki skimu hii ipate basi hela hata kidogo ili ianze kutengenezwa ianze kujengwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru nimeona skimu ya Nyanzwa imetajwa kwa ajili ya tathmini ya mazingira. Nimesoma ukurasa wa 82 mpaka 84 wa randama nikaona chini kuna kujenga skimu 14 na hazijatajwa. Kwa hiyo, kwa sababu tathmini yamazingira inafanyika Nyanzwa na pale chini kuna skimu 14 zitafanyika ukurasa 82 hadi 83 wa randama, naomba Nyanzwa iwemo mojawapo kati ya zile 14 ambazo nimeziona pale kwenye randama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo jingine ambalo ningependa kuliongelea hapa, Mheshimiwa Waziri umesimama hapa mara nyingi sana kukemea suala la lumbesa, watu wa kule tunalima mboga mboga horticulture, nakukumbusha kwamba korosho inapimwa kwa kilo huwa aina lumbesa, kawaha inapimwa kwa kilo huwa aina rumbesa, pamba inapimwa kwa kilo huwa haina lumbesa. Sasa tuje kwetu vitunguu tunavyolima vina lumbesa, nyanya tunazolima wanajua wenyewe wananvyopanga, tuje viazi vina lumbesa, mazao yote ya mboga mboga yana lumbesa, umekemea mara nyingi hapa kama imeshindikana itungwe sheria mahsusi ya vipimo vya mazao ya kilimo ili wale wananchi waweze kunufaika na kilimo chao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni kulikuwa na zao la pears, matunda tu ya kawaida na nilifika kule Kijiji kimoja cha Ilamba, tenga moja ni kama matenga matatu, mtu anaweka mpaka atakapoamua mwenyewe ni Shilingi Elfu Kumi, lakini ni kwa sababu hakuna kipimo madhubuti kinachotumika kupima yale mazao. Ninakuomba sana pamoja na kukemea huko bado tatizo hili ni kubwa, ninakuomba tuangalie namna gani tutawakomboa wakulima wanaolima mazao ya mboga mboga ili na wao waweze kujikomboa kama haya mazao mengine yalivypata ufumbuzi kwenye suala zima la lumbesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na ninaunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Hoja ya Kuazimia Kuwahamisha Maafisa Ushirika katika Tume ya Maendeleo ya Ushirika na Maafisa Ugani chini ya Wizara ya Kilimo
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuwa mchangiaji wa kwanza wa hoja hii.

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa ugatuaji wa madaraka ulipangwa kulenga kuendelea kuzipa nguvu Halmashauri kujisimamia na kusimamia shughuli zake. Kumekuwa na utaratibu wa kunyofoa vipande mbalimbali ndani ya Mamlaka za Halmashauri. Ilianza Ardhi kidogo, TARURA ikatolewa, ikaja Ardhi imetolewa, Maji imetolewa na kila moja inatolewa kwa namna yake kwa hoja mbalimbali zinazoletwa hapa ndani, ikiwa utaratibu huu utaendelea maana yake ni kwamba mwisho Halmashauri zitabaki bila Idara yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, inawezekana kukawa na mapungufu katika utekelezaji, nadhani ni vema tukaangalia namna bora ya kuimarisha Halmashauri zetu na usimamizi wake, hata hizi zilizotolewa zikaangaliwa jinsi gani Halmashauri zinaweza zikawa na udhibiti badala ya kuendelea kunyofoa kila kipande na mwisho tukaacha Halmashauri hazina kitu chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja iliyowasilishwa inaweza ikawa na mashiko, udhaifu kwenye Ushirika unaweza ukawepo, kwa hiyo siyo kwamba napinga kwamba kwenye Ushirika kuna changamoto, najua zinaweza zikawepo lakini suluhisho lake si kuendelea kunyofoa Idara katika Halmashauri na mwisho wake kuacha Halmashauri hazipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama tuna mashaka na jinsi tulivyofanya ugatuaji wa madaraka ni bora tufute sasa hizo Halmashauri zisiwepo kuliko kila siku unatoa kipande hiki, unatoa kipande hiki, mwisho unaimaliza Halmashauri kwa hiyo itakuwa na Mkurugenzi tu.

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi nilikuwa naomba…

SPIKA: Mheshimiwa Justin Nyamoga kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kwezi.

TAARIFA

MHE. ALOYCE A. KWEZI: Mheshimiwa Spika, nilitaka nimpatie taarifa mzungumzaji kwamba hata baada ya kuwa wamechukua baadhi ya watumishi kwenye Idara hizo alizozitaja, kwa maana ya Ardhi, Maji na TARURA imetuwia vigumu sana Madiwani. Kwanza imekuwa ni kama hisani kwa hiyo utendaji wa kazi wa Madiwani ambao ndio wanatakiwa kutafsiri miradi na mambo yote yanayoendelea kwa faida ya nchi yamekuwa magumu sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nataka nimpe taarifa hiyo. (Makofi)

SPIKA: Haya, ahsante sana Mheshimiwa Kwezi ulikuwa unatoa taarifa siyo unachangia. Mheshimiwa Nyamoga unapokea taarifa hiyo?

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ninaipokea taarifa na mimi hoja yangu kwa kweli kwenye hili nafikiri tujenge mifumo mizuri ya ugatuaji wa madaraka, tuimarishe Halmashauri na hata hizi ambazo tumezitoa tutafute namna bora ya kujenga uhusiano na Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, maji, barabara na zingine zisimamiwe vizuri lakini Halmashauri ziwe na uwezo lakini tusiendelee kunyofoa moja baada ya nyingine.

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, taarifa

SPIKA: Mheshimiwa Nyamoga, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mbunge wa Manonga.

TAARIFA

MHE. SEIF K. S. GULAMALI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Napenda kumpata taarifa mchangiaji, tumeona ugatuaji katika Halmashauri zetu kwa mfano TARURA toka ilipowekwa mamlaka yake, sasa hivi inafanya vizuri zaidi tofauti na ilivyokuwa mwanzo. Kwa hiyo, hawa Maafisa wetu wakati mwingine wakiwa Halmashauri hata mafuta hawana. Naomba kuwasilisha. (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana. Mheshimiwa Justin Nyamoga unapokea taarifa hiyo.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, hata sijaelewa, kwa hiyo sitapokea. (Kicheko/Makofi)

SPIKA: Sawa. Sasa ukisema hujaelewa, hujamsikia ama hoja yake huikubali? Kwa sababu sasa…

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, sijamsikia.

SPIKA: Basi wacha nikueleweshe, anasema hivi: Imetolewa mifano ya TARURA, TARURA ilivyoondolewa Halmashauri yeye kwa taarifa anayokupa ni kwamba ufanisi umeongezeka. Kwa hiyo, unaipokea taarifa hiyo? Ndiyo taarifa ya Mheshimiwa Mbunge.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, kuhusu ufanisi kuongezeka napokea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni kwamba kuna haja ya kuboresha Halmashauri zetu ziwe na usimamizi, ziwezeshwe, hata kwenye hilo suala la ushirika ukiangalia changamoto utaenda kukuta si kwamba kwa sababu iko kwenye Halmashauri, utakuta kuna matatizo ya kibajeti, utakuta kuna matatizo ya kiutawala na utakuta kuna matatizo mengine na siyo suala la kiutawala. (Makofi)

SPIKA: Haya, kengele ya pili imegonga Mheshimiwa.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana.

SPIKA: Kengele ni moja, samahani kengele imegonga.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi.

SPIKA: Shukrani.

MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, kwa hili siwezi kuunga mkono hoja iliyowasilishwa. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan pamoja na Serikali yake ya Awamu ya Sita kwa jinsi ambavyo inaendelea kutekeleza Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi. Nitahitaji karibu siku nzima kutaja miradi ambayo iko katika jimbo langu, kwa hiyo itoshe kusema tunamshukuru sana na tunaendelea kushukuru kwa niaba ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuzungumzia miundombinu ya barabara na nimwombe Mheshimiwa Waziri kwamba wakati wa kusoma bajeti alitaja barabara kadhaa. Nitamweleza hii barabara na anahitaji tu kuiongeza, haiongezi fedha kwenye bajeti yake tayari ipo. Barabara ya kutoka Iringa kwenda Kilolo ambayo itajengwa kwa kupitia fedha za Rais. Nimejiridhisha na TANROADS kwamba ipo kwenye taratibu za kuandaliwa tenda, lakini wananchi wa Kilolo waliniuliza kwamba kwa nini Waziri hakuitaja. Basi kwenye hitimisho Mheshimiwa Waziri aitaje tu kwa sababu tayari iko kwenye mipango ili wananchi waweze kuelewa kwamba ni mojawapo ya barabara zitakazotengenezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kiutaratibu magari yetu huwa yanakuwa na spare tyre kwa maana kwamba kukitokea dharura basi ile tairi inasaidia kufunga na kuondoka. Barabara ya kutoka Dar es Salaam hadi Mbeya, Tunduma na inayoenda Kyela ipo sehemu moja yenye shida kubwa ambayo huwezi kuchepuka kwa namna yoyote ile na hii ni ile sehemu ya Mlima Kitonga na nimeitaja mara nyingi hapa. Naomba nisikilizwe kwa sababu ni kwa maslahi ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukifika pale kama kukitokea gari ikaharibika kwa sababu zile kona ni nyingi na mara nyingine magari kupinduka na hayo ni matukio ya mara kwa mara, hakuna njia nyingine, kwa maana nyingine barabara ile inakuwa imefungwa na hakuna pakupita. Maana yake ni kwamba lazima kutafuta mbadala ili magari yaweze kuzunguka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi karibuni kulitokea tukio kama hilo na wakati napita pale Ilula kulikuwa na ambulance tatu kutoka Mbeya na kutoka Iringa ambazo zilikuwa zinaelekea Dar es Salaam zina wagonjwa ndani. Kama hiyo haitoshi hivi karibuni kutoka Ruaha Mbuyuni kwenye Kituo cha Afya kuna mama mmoja ambaye alikuwa wa kujifungua, alifia pale kwa sababu tayari kulikuwa kumezibwa ile njia pale. Hayo ni matukio ya kiafya, lakini bado hatujazungumzia madhara ya kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkuu wa Mkoa alishawahi kukwama pale, wako Mawaziri walishawahi kukwama pale na Mheshimiwa Waziri wa Fedha asisubiri aje akwame pale ndipo aseme, alichokuwa anasema Mheshimiwa Mbunge kilikuwa cha muhimu. Niombe barabara ya mchepuko ambayo nimesema kwamba tumeshaanza kuitengeneza kwa kupitia fedha za UVIKO kutoka Mahenge kwenda Udekwa, inapita inatoka pale Ilula ni kilomita chache sana na ikitengenezwa itakuwa ukombozi kunapotokea tatizo pale. Niombe sana hilo liangaliwe ili liweze kufanyiwa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo napenda kuzungumzia ni suala la lumbesa. Nalo nimeshalipigia kelele sana hapa. Mheshimiwa Waziri inabidi aelewe kwamba waitazame kwa lenzi ya kimapato. Sisi mapato ya halmashauri tunakusanya kwa kuhesabu magunia. Magunia mawili yanazalisha gunia lingine moja, maana yake ni kwamba wanapofika kule ukiwa na gunia, ukiwa unakusanya shilingi bilioni tatu maana yake ni kwamba umepoteza shilingi bilioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kila halmashauri kama tukihesabia magunia kwa vipimo vinavyotakiwa, halmashauri zingepata mapato moja ya tatu zaidi wanayopata sasa hivi, lakini tukizungumza kwa lenzi ya hasara wanayopata wakulima, nimeshalisema sana kwa sababu hamna kipimo kinachotumika. Tuangalie kwa lenzi ya kimapato, tunaweza tukaelewa ni mapato kiasi gani halmashauri zinapoteza kwa sababu tu suala la lumbesa linaonekana limeshindikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, siamini kwamba Serikali imeshindwa kufanya udhibiti wa suala la lumbesa. Tungependa sisi wakulima wa kutoka Kilolo, Makete na mikoa mingine ambayo tunazalisha viazi, njegere na hivyo vyote visivyokuwa na vipimo, tunapenda kujua Serikali ina mikakati gani ya kukomesha tatizo la lumbesa ambalo linawaumiza sana wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niende kuzungumzia suala la ada. Elimu yetu inaenda kama pyramid, huku chini wanafunzi wengi wanakuwa shule ya msingi baadaye wanaenda sekondari, baadaye chuo. Wanapofika Chuo Kikuu wanakuwa ni wachache sana, sasa mtu ameshindwa kulipa 20,000 tumesema elimu bure, mtu ameshindwa kulipa 70,000 tumesema elimu bure, huyu mtu anamfikisha mtoto wake Chuo Kikuu tunasema alipe shilingi laki saba anatoa wapi?

Mheshimiwa Naibu Spika, pendekezo langu pamoja na kuweka dirisha maalum la kusaidia watu, iangaliwe namna ya watu ambao hawawezi kulipa ada za Vyuo Vikuu. Nimekusanya takwimu kwa mwaka mmoja kwenye Jimbo langu, wanafunzi walionijulisha kwamba wanaahirisha masomo ninao wanafunzi 14 kutoka vyuo mbalimbali walioahirisha masomo kutoka vyuo vya Serikali, kwa sababu hawakuweza kumudu kulipa ada kwenye vyuo vikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia vyuo vya Kati imesemwa sana niombe kwa sababu tangu nimeingia Bunge hili tunazungumzia vyuo vya kati, watoto wale nao ni wa Watanzania, hatuwezi kuwa na watu wenye digrii watupu, nao waingizwe kwenye elimu bure kwa sababu wana haki kama wanaoenda vyuo vikuu. Nina uhakika na wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Spika na wengine wote tukipata shida za mifumo ya maji kwenye nyumba zetu hata leo, tunawaita hawa hawa ambao tunawakandamiza kwamba walipe ada na tunajua wametoka kwenye familia maskini, hili halikubaliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalize kwa kuzungumzia mikopo ya vifaa vya usafiri na kukumbusha tu, kwamba uendeshaji wa Serikali pia unaanzia kwenye ngazi za chini hasa kwa mfano ngazi ya Kata, ambapo tunao Watendaji wa Kata. Ukiangalia sekta nyingine kama kilimo, mifugo na idara nyingine zimeanza kuangalia sekta ya Kata, lakini ujumla wake wale Watendaji wa Kata wenyewe hawana vitendea kazi, hawana pikipiki. Sasa mtakapoanza kutoa vifaa hivi kwa utaratibu wowote mtakaoweka, kumbukeni kwamba ile miradi tunayoipelekea fedha nyingi, wanaoisimamia katika ngazi ya kwanza ni Watendaji wa Kata. Hivyo wakumbukwe ili waweze pia na wao kupatiwa vifaa vya usafiri weweze kuhudumia jamiii yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkona hoja. (Makofi)