Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon Omary Juma Kipanga (4 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa fursa ya kuchangia hoja hii. Wachangiaji wengi wakati wakisimama hapa walikuwa wana-declare interest na wengi wao walikuwa ni walimu, na nimepata bahati ya kufanya kazi sasa na walimu, naomba ni-declare interest ya professionalism yangu, by profession ni Quantity Surveyor, kwa maana ya kwamba ni QS.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo sasa naomba nichangie hoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda kutumia fursa hii adhimu na adimu kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenijalia afya njema na leo nimepata fursa ya kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia namshukuru Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kuniamini na kuniteua katika nafasi hii. Ninampongeza kwa kazi kubwa anayoifanya katika kuwaletea maendeleo Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, sina budi kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushauri na maelekezo yao muhimu katika utekelezaji wangu wa majukumu ya kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kukushukuru wewe na Mheshimiwa Spika kwa kuliongoza Bunge hili kwa hekima, busara na weledi mkubwa. Naishukuru pia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa ushirikiano mkubwa wanaotupatia; hii ni moja ya Kamati bora sana ambayo Wajumbe wake wana uelewa mpana katika sekta ya elimu na hivyo kuendelea kutoa ushauri muhimu katika kuboresha Sekta ya Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kumshukuru Mheshimiwa Prof. Joyce Lazaro Ndalichako, Mbunge, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, kwa uongozi wake thabiti ndani ya Wizara. Pia namshukuru Katibu Mkuu, Dkt. Akwilapo; Naibu Makatibu Wakuu na watendaji wote wa Wizara kila mmoja kwa nafasi yake, kwa ushirikiano wanaonipa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho lakini siyo kwa umuhimu, naishukuru familia yangu kwa upendo na ushirikiano mkubwa wanaonipatia katika utekelezaji wa majukumu yangu. Pia nawashukuru sana wapigakura wangu wa Jimbo la Mafia kwa imani yao kubwa kwangu na ushirikiano ambao umesaidia jimbo letu kupiga hatua kubwa katika kipindi cha Awamu ya Tano na ya Sita ya Serikali yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya shukrani hizo sasa naomba kutoa ufafanuzi kwa baadhi ya hoja ambazo zimechangiwa na Waheshimiwa Wabunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu umuhimu wa sayansi teknolojia na ubunifu; Waheshimiwa Wabunge wengi walionesha umuhimu wa kuendeleza sayansi, teknolojia na ubunifu kwa ajili ya maendeleo ya nchi. Serikali inatambua umuhimu wa mchango wa ubunifu na teknolojia katika kurahisisha na kuongeza ufanisi wa utekelezaji wa shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii na ni nyenzo ya kichocheo cha maendeleo ya haraka katika sekta ya huduma za jamii na uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanzisha Mashindano ya Kitaifa ya Sayansi, Teknolojia na Ubunifu (MAKISATU) kwa lengo la kuibua, kutambua na kuendeleza ubunifu na ugunduzi wa teknolojia mbalimbali unaofanywa na Watanzania, hususan wale wa ngazi za chini. Mashindano haya yanawapa nafasi wabunifu na wagunduzi wa teknolojia kujitangaza na hivyo kujulikana na wadau wa ubunifu unaozalishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tangu kuanza kwa mashindano haya mwaka 2019, Serikali imefanikiwa kuibua na kutambua wabunifu wachanga 1,780 kati ya hao, wabunifu mahiri 1,030 wameendelezwa na Serikali ili ubunifu na teknolojia walizoanzisha zifikie hatua ya kubiasharishwa na hivyo kuongeza fursa za ajira kwa vijana na kuchangia kwenye Pato la Taifa. Aidha, Serikali kupitia COSTECH imeanzisha vituo atamizi 17 kwa ajili ya kukuza na kuendeleza ubunifu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu Serikali kuongeza vyuo vya VETA kwa kila mkoa na wilaya; Serikali ina mpango wa kuhakikisha kunakuwepo na Chuo cha Ufundi Stadi katika kila mkoa na wilaya nchini. Kwa sasa vyuo 42 vinaendelea na mafunzo, pamoja na hivyo, Serikali inaendelea na ujenzi wa vyuo 29 vya wilaya na vyuo vine vya ufundi stadi vya mikoa ambavyo vipo katika hatua mbalimbali za ujenzi. Hata hivyo, Serikali itaendelea na utekelezaji wa ujenzi wa vyuo vya VETA vya wilaya kwa kadri fedha zitakavyopatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu Wizara kuboresha vyuo vya ufundi ili viweze kuendana na maendeleo ya sayansi, teknolojia na ubunifu. Serikali inaendelea na kuboresha na kuimarisha vyuo vya ufundi kwa kuboresha miundombinu ya kufundishia na kujifunzia pamoja na kununua vifaa na mitambo ya kisasa. Kwa sasa Serikali kupitia mradi wa A STRIP inaendelea na ujenzi wa vituo mahiri (Centers of Excellence) katika Chuo cha Ufundi Arusha, Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam katika Kampasi za Dar es Salaam na Mwanza na Chuo cha Taifa cha Usafirishaji (NIT) katika Nyanja za nishati, usindikaji wa ngozi, usafiri wa anga na TEHAMA.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kukamilika, vyuo hivi vitakuwa na hadhi ya kimataifa vinavyoweza kutoa ujuzi unaoendana na soko la ajira na hivyo kuvutia wanafunzi wa ndani na nje ya nchi. Serikali itaendelea kutenga fedha kwa ajili ya kuboresha vyuo vingine vya ufundi nchini katika bajeti yake ya maendeleo ili kuhakikisha vyuo hivyo vinatoa elimu stahiki inayoendana na mahitaji ya soko la ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu Serikali kuwa na utaratibu w akufanya ufuatiliaji wa wahitimu baada ya kumaliza masomo (tracer study); Serikali impokea maoni na itaendelea kuhakikisha kuwa ufuatiliaji wa wahitimu unafanyika na unakuwa endelevu ili utumike katika kuboresha mitaala ya mafunzo na hivyo kukidhi mahitaji ya soko.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, vyuo vikuu mbalimbali, Baraza la Elimu ya Ufundi (NACTE), Mamlaka ya Ufundi (VETA) na Taasisi ya Sekta Binafsi (Tanzania Private Sector Foundation) na mamlaka nyingine nchini hufanya tracer studies mara kwa mara kwa baadhi ya fani ili kupata taarifa za wahitimu hao, waajiriwa na waliojiajiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja kuhusu Serikali kuwa na utaratibu wa kufanya utafiti wa soko la ajira ili kubaini mahitaji…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, kengele imeshagonga.

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kipengele cha mwisho cha udhibiti ubora; Serikali kupitia miradi yake ya kuendeleza elimu Lens na imekuwa ikituwezesha idara ya udhibiti ubora wa shule kutekeleza majukumu yake kwa kufanya yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeongeza bajeti ya wadhibiti ubora kutoka bilioni 5.2 mpaka bilioni 5.7.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja, nawashukuru sana kwa kunisikiliza, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Awali ya yote, napenda kuchukua fursa hii adhimu na adimu kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa kibali cha kusimama mchana huu wa leo mbele ya Bunge lako Tukufu nami niwe miongoni mwa watu wa kuchangia hoja hii ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nichukue fursa hii vilevile kumpongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakati akihutubia Bunge tarehe 22 mwezi wa Nne mwaka 2021 alielekeza mambo mbalimbali ambayo sisi Wizara ya Elimu tunapaswa kuyafanyia kazi; kipekee mwezi wa 10 alipopata fedha zile za UVIKO -19 zaidi ya Shilingi bilioni 304 ambazo aliweza kuzielekeza kwenye sekta ya elimu. Kwa hiyo, katika maono hayo na ndoto hizo hatuna budi kumpongeza kwa karibu sana Mheshimiwa Rais kwa juhudi kubwa.

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nichukue fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini, kuweza kumsaidia kuhudumu katika Wizara hii ya Elimu nikishirikiana kwa karibu na Mheshimiwa Prof. Mkenda. Vile vile napenda kuchukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Prof. Mkenda, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Katibu Mkuu, Prof. Sedoyeka, Manaibu Makatibu Wakuu, Wakurugenzi, Wakuu wa Taasisi na Watumishi wote wa Wizara ya Elimu kwa ushirikiano wa karibu wanaonipa katika kutimiza majukumu yangu ya kila siku.

Mheshimiwa Spika, kipekee nichukue fursa hii vilevile kuwashukuru sana wananchi wa Jimbo la Mafia kwa imani yao kubwa na ushirikiano wanaonipa katika kuleta maendeleo katika Jimbo letu la Mafia na kuendelea kushirikiana na kunivumilia katika kipindi hiki chote wakati natekeleza majukumu haya. Mwisho, lakini siyo kwa umuhimu, familia yangu niweze kuishukuru kwa upendo pamoja na ushirikiano na uvumilivu walionionesha katika kipindi hiki chote.

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nikushukuru wewe Spika pamoja na Naibu Spika na Wabunge wote kwa ushirikiano mnaotupa Wizara ya Elimu wakati tunaendelea kutekeleza majukumu haya muhimu ya Taifa. Baada ya shukrani hizo, sasa naomba nijikite kwenye maeneo machache ambayo ni ya kutoa ufafanuzi kwenye baadhi ya hoja ambazo Waheshimiwa Wabunge wameendelea kutoa tokea jana mpaka siku ya leo mchana.

Mheshimiwa Spika, naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge, maoni yenu yote pamoja na mawazo mliyotupa pamoja na mapendekezo, tumeyabeba, tunayachukua, tunaenda kuyafanyia kazi. Vilevile kutokana na muktadha wa muda, tusingeweza kujibu hoja zote hapa leo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikuhakikishie tu kwamba hoja hizi tutazileta kwako kwa maandishi ili ziweze kuwa rejea na kumbukumbu sahihi ya kikao hiki pamoja na Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, eneo la kwanza ambalo ningependa kutolea ufafanuzi ni eneo la lishe mashuleni. Imezungumzwa hapa kwamba bila lishe na chakula shuleni inawezekana tendo la kujifunza shuleni likawa gumu. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu, Waraka wa Elimu Na. 3 wa Mwaka 2016 unafafanua vizuri jambo hili la ushirikishwaji wa jamii kwenye eneo la elimu na utoaji wa lishe pamoja na chakula shuleni. Vilevile mwaka huu 2022 sisi kama Wizara tumeweza kutoa mwongozo wa namna gani jamii pamoja na wadau mbalimbali tunaweza tukashirikiana kwa pamoja ili kuhakikisha kwamba tunakwenda kutoa chakula shuleni.

Mheshimiwa Spika, hivi sasa Wizara yetu ipo kwenye mchakato wa kuhakikisha kwamba tunaenda kutengeneza mpango mkakati namna gani tunatekeleza mwongozo huu. Vilevile tayari tumeshaingia makubaliano na wenzetu wa World Food Program kuhakikisha kwamba kuna maeneo ambayo tunakwenda kuyafanyia kazi na kuona ni namna gani tunaweza tukatekeleza mpango huu wa kuweza kuweka chakula shuleni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge tunakoelekea ni kuzuri, lakini hili litakuwa na matokeo chanya ikiwa tu tutaweza kushirikiana kwa pamoja kwa sababu, ushirikishwaji wa jamii kwenye jambo hili la utoaji wa chakula shuleni ni jambo la msingi sana kwa sababu, tumeweza kufanya kama pilot kwenye Mikoa ya Njombe pamoja na Kilimanjaro na Mara na imeonesha matokeo chanya. Sasa matokeo yale tuliyoyapata kwenye pilot hiyo yatatusaidia sasa kuenea mpango huu kwenye mikoa yote nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitoe wito wa ushirikiano, na vilevile tumepanga kuweka kikao kikubwa sana na wadau wote wa elimu kuhakikisha tunakwenda kujadili namna gani mpango huu tunaweza tukautekeleza kwa vitendo kwa manufaa mapana ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hilo ni eneo la kwanza nikasema angalao tunaweza tukalitolea ufafanuzi wa kina.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo ningependa kulitolea ufafanuzi ni la udhibiti ubora wa shule. Katika eneo hili, ni kweli tunafahamu umuhimu wa udhibiti wa ubora ili kuweza kulinda ubora wa elimu yetu nchini. Kwa kuzingatia azma hiyo, Serikali imejielekeza na kuweka mifumo sahihi, nguvu kazi pamoja na vitendea kazi ili kuhakikisha kwamba eneo hili la udhibiti ubora tunakwenda kulifanyia kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki Serikali imeweza kufanya majukumu kadhaa kuhakikisha eneo hili la wadhibiti ubora linakwenda kukaa sawasawa. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2018/2019 mpaka 2021/2022 Serikali imeweza kununua magari zaidi ya 84 na kuyasambaza kwenye ofisi zetu za kanda pamoja na zile za Halmashauri ikiwa ni eneo la vitendea kazi kama nilivyozungumza pale mwanzo. Vilevile tumeweza kujenga ofisi kwenye maeneo au Halmashauri ambazo zilikuwa hazina ofisi kabisa, zaidi ya ofisi 155 zimeweza kujengwa kwenye Halmashauri mbalimbali nchini ili kuweza sasa kutengeneza mazingira mazuri ya wadhibiti ubora kuweza kufanya kazi zao vizuri na katika mazingira mazuri na salama.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Serikali imetumia zaidi ya Shilingi bilioni 2.6 kwa ajili ya kufanya M and E kwa maana ya Monitoring and Evaluation, na kuwafundisha wadhibiti ubora namna bora ya kuweza kwenda kufanya kaguzi mbalimbali kwa ajili ya kudhibiti taratibu za ufundishaji na kujifunza kwenye maeneo ya shule zetu. Pia tumeweza vilevile kufanya ukarabati wa ofisi zaidi ya 31 kwenye maeneo mbalimbali nchini. Tumeweza vilevile kuongeza watumishi kwenye eneo hilo la wadhibiti ubora ambapo zaidi ya watumishi wapya 619 wameweza kupelekwa kwenye ofisi mbalimbali kwa lengo la kuhakikisha ofisi zinapata rasilimali watu wa kuweza kufanya majukumu hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa vitendea kazi, tumenunua vishikwambi au kompyuta mpakato 867, kwa sababu tunajua sasa hivi taratibu na mifumo ndiyo ambayo inafanya kazi zaidi kuliko taratibu za zamani zile za makaratasi. Kwa hiyo, tumeweza kujikita kwenye upande wa mazingira pamoja na vitendea kazi na tunaendelea kufanya maboresho makubwa kwenye eneo hili pamoja na utoaji wa mafunzo kwa wadhibiti ubora ili kuhakikisha kwamba kazi zao wanakwenda kuzifanya sawasawa.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo napenda kutolea ufafanuzi au hoja nyingine ni ya miundombinu. Imezungumzwa sana hapa kuhusiana na suala la miundombinu hasa kwa watoto wetu wenye mahitaji maalum. Naomba nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba katika kuhakikisha taasisi za elimu zinakuwa na miundombinu rafiki kwa makundi yote, Wizara imeandaa mkakati wa ujenzi na utunzaji wa shule unaoitwa School Construction and Maintenance Strategy. Mkakati huu ni wa miaka 10 wa 2019 mpaka 2028 ambao unabainisha viwango vya kuzingatia wakati wa ujenzi na utunzaji wa majengo ya shule pamoja na vyuo mbalimbali ikiwemo kuweka miundombinu ya kuzingatia wenzetu wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, eneo hili hata ukienda sasa hivi kwenye madarasa yetu tunayojenga kwamba, ni lazima zile ramp nazo ziweze kuonekana kwenye maeneo hayo ili kurahisisha wenzetu au watoto wetu wenye mahitaji maalum waweze kufanya mizunguko pamoja na kuingia na kutoka darasani bila changamoto yoyote.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ililetwa mezani hapa nadhani ni muhimu kuitolea ufafanuzi, ni suala la uanzishwaji wa madawati ya jinsia katika ngazi zote za elimu. Jambo hili tayari Wizara tumeshalifanyia kazi, lipo na ilikuwa ni suala tu la utekelezaji. Kwa mujibu wa Waraka wa Elimu Na. 11 wa Mwaka 2002, ulikuwa unaeleza wazi kwamba katika kila shule zetu za msingi na sekondari, kulikuwa kunahitajika au inapaswa kuwa na walimu wanasihi angalao wawili, yaani wa kike mmoja na mwanaume mmoja ambao wataunda Kitengo cha Malezi, Ushauri, pamoja na unasihi shuleni. Kwa hiyo, tunakwenda kusimamia vizuri mwongozo huu, lakini kazi za walimu hawa sasa zimebainishwa waziwazi katika waraka huo.

Mheshimiwa Spika, kazi za walimu hawa wa malezi ni kutoa huduma ya malezi pamoja na unasihi kwa wanafunzi, ikiwa ni pamoja na kuwasaidia kukabiliana na changamoto mbalimbali za kimaisha zinazoweza kuathiri kisaikolojia na kiafya ambazo hatimaye huathiri namna ya kujifunza. Kwa hiyo, tunakwenda kusimamia vizuri mwongozo pamoja na waraka huo kuhakikisha kwamba, eneo hili nalo linakaa sawasawa.

Mheshimiwa Spika, naomba nikuhakikishie Wizara ya Elimu kwa kushirikiana na Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, imeandaa mwongozo wa uandaaji wa madawati haya ya ulinzi na usalama wa watoto ndani na nje ya shule ambapo waraka huu ni wa mwaka huu 2022. Madawati hayo yatafanya kazi chini ya walimu walezi ili kudhibiti matukio ya ukatili na unyanyasaji dhidi ya watoto ndani na nje ya shule. Kwa hiyo, tunakwenda kusimamia vizuri waraka huu kuhakikisha vitendo hivi vya unyanyasaji kwa namna yoyote ile tunakwenda kuvikomesha kwenye maeneo yetu ya kujifunzia.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine lililozungumzwa sana hapa ni eneo la ujenzi wa Vyuo vya VETA nchini ambalo ndilo tunaloendeleanalo hivi sasa. Naomba niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Bunge lako Tukufu, kazi hii inakwenda kwa speed kubwa. Naomba nitoe takwimu hapa kwamba mpaka kufika mwezi Juni, mwaka huu 2022 jumla ya Halmashauri au jumla ya Wilaya 77 zitakuwa zimepata vyuo hivi vya VETA. Kwa hiyo, safari yetu itakuwa imebaki kidogo tu kwenye Halmashauri zile nyingine ambazo zitakuwa zimebaki. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaondoe wasiwasi ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali yetu ya Awamu ya Sita imejizatiti kuhakikisha kwamba eneo hili tunakwenda kulifanyia kazi sawasawa. Kwa hiyo, niwaondoe wasiwasi na sisi tutakwenda kusimamia eneo hili kwa umahiri mkubwa sana kuhakikisha kwamba mambo haya yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, imezungumzwa kidogo kuhusiana na ujenzi wa Chuo cha Mkoa cha Geita. Nimwondoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, ujenzi unaoendelea pale ni ujenzi ambao ni sahihi zaidi kwa sababu tumekwenda kuongeza hata miundombinu mingine ambayo ilikuwa haipo. Ujenzi ule wa mwanzo wakati unajengwa na mkandarasi mfano vitu kama mabweni yalikuwa mawili tu, bweni moja kwa wasichana na bweni moja kwa wavulana, lakini ujenzi wa sasa hivi tunaofanya tumeongeza mabweni mengine mawili kwa maana yatakuwa mawili ya wasichana na mengine ya wavulana.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, amezungumza kwamba, ujenzi wakati unafanywa na mkandarasi ilikuwa ni zaidi ya Shilingi bilioni 14 zingetumika kwa ajili ya ukamilishaji wa ujenzi ule, lakini kwa kutumia Force Account tunakwenda kutumia Shilingi bilioni tano na itakamilisha ujenzi ule, lakini kwa kuongeza miundombinu mingine rafiki. Kwa hiyo, siyo tu kwamba tumepunguza gharama za ujenzi, bali vilevile tumeboresha mazingira yale. Nimwondoe wasiwasi kwamba chuo kile kitakuwa ni miongoni mwa vyuo vizuri vya mikoa hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, pia alisema kuna zile structure ambazo zinanyanyuliwa sasa hivi ambazo ni steel structure. Kwenye frame structure tuna namna mbili ya kujenga; tunaweza tukatumia concrete structure au tukatumia steel structure, lakini zinafanya kazi hiyo hiyo. Kwa hiyo, nimhakikishie tu kwamba ubora wa chuo kile unakwenda kuwa vizuri kabisa na gharama yake inakuwa ni ya chini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo, naomba niunge mkono hoja ya Mheshimiwa Waziri. Naomba tu Waheshimiwa Wabunge muweze kutupitishia bajeti yetu hii ili tuweze kuunga mkono juhudi za dhati za Mheshimiwa Rais za kuhakikisha kwamba tunakwenda kufanya restructuring katika mfumo wetu wa elimu ili hiyo Tanzania anayoihitaji Mheshimiwa Rais tuweze kuifikia.

Mheshimiwa Spika, ahsanteni sana, naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii adhimu na adimu, kwanza kabisa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu aliyenipa kibali mimi pamoja na ninyi tukaweza kukutana, lakini vile vile tukaweza kujadili hoja iliyokuwa mbele yetu.

Mheshimiwa Spika, kipekee nishukuru kuwa mmoja miongoni mwa wachaingiaji wa hoja hii iliyokuwa mezani ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. Pili, nichukue nafasi hii kipekee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kutuamini mimi na Profesa Mkenda kuweza kutupa mamlaka na madaraka ya kuweza kushiriki kwenye uongozi wa Wizara yetu ya Elimu, Sayansi na Teknolojia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa ushirikiano, kwa maelekezo, kwa miongozi mbalimbali ambayo imeniwezesha kushiriki lakini vile vile kuweza kuongoza Wizara hii. Vile vile nimshukuru sana Katibu Mkuu, Profesa Nombo, Naibu Makatibu Wakuu, Kamishna wa Elimu, Wakurugenzi wote na Menejimenti nzima ya Wizara ya Elimu pamoja na taasisi zilizokuwa chini ya Wizara ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nikushukuru wewe binafsi kwa kuliongoza Bunge letu, Naibu Spika, Wenyeviti wa Bunge lakini vile vile na Kamati yetu ya Elimu na Wabunge wote. Tunawashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa ushirikiano ambao wanaotupa ili kuweza kurahisisha majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee naomba nichukue fursa hii vile vile kuwashukuru sana wananchi wangu, wapiga kura wangu wa Jimbo la Mafia. Kwanza kwa kuniamini, lakini pili kwa kuendelea kunipa ushirikiano. Pamoja na majukumu mengine haya ya Kiserikali lakini bado jimboni kule salama na kila nikienda wananipa ushirikiano wa kutosha ndani ya chama pamoja na wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho, naomba niishukuru sana familia yangu kwa kuwa karibu na mimi katika kipindi chote wakati natekeleza majukumu yangu. Tunashukuru kwa hoja ambazo tumezipata, tumezipokea. Nichukue fursa hii niwatoe wasiwasi na hofu Waheshimiwa Wabunge kwa yale yote ambayo wamechangia kwenye Wizara yetu, tutakwenda kuyasimamia. Kuna maeneo ya ushauri, kuna maeneo ya maelekezo, lakini kuna maeneo ya maagizo na kuna maeneo vile vile vya marekebisho. Tutakwenda kuyasimamia haya yote waliyoyapendekeza katika utekelezaji wetu wa bajeti katika mwaka ujao wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba sasa uniruhusu nami niweze kuchangia kwenye baadhi ya maeneo katika hoja iliyopo mbele yetu. Eneo la kwanza naomba kuchangia kwenye eneo la ujenzi wa vyuo vyetu vya VETA.

Mheshimiwa Spika, kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi nafahamu iko Ibara ambayo inazungumzia Serikali itakwenda kujenga vyuo vya VETA kwa lengo la kusogeza huduma ya elimu haswa ya ufundi karibu na wananchi na Serikali imejidhatiti kuhakikisha kwamba tunajenga.

Mheshimiwa Spika, tulianza ujenzi huu karibu miaka miwili iliyopita katika mwaka wa fedha 2020/2021 lakini tumeweza kuendelea nao katika mwaka 2021/2022 tumeweza kujenga vile vyuo 25 katika Wilaya 25 nchini lakini baadae na vile vyuo vinne vya Mikoa. Katika mwaka huu wa fedha tumeweza kuanza ujenzi katika Wilaya zile 64 ambazo zilikuwa hazina vyuo vya VETA na katika Mkoa mmoja wa Songwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaondoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge tutaenda kusimamia eneo hili kwa uadilifu na uaminifu mkubwa,tayari shughuli za ujenzi kule zimeshaanza. Tunafahamu ziko Wilaya ambazo zina Majimbo zaidi ya moja, kulitokea malalamiko mengi humu kwamba tunakwenda kujenga katika Wilaya na siyo katika Majimbo. Niwaondoe hofu Waheshimiwa Wabunge tunajua kuna baadhi ya Majimbo, tunajua kuna baadhi ya Halmashauri zimetenga maeneo kwa ajili ya ujenzi wa vyuo hivi lakini categorically tulisema kwamba tunakwenda kujenga katika Wilaya na siyo Halmashauri au Jimbo.

Mheshimiwa Spika, niwaondoe hofu tumepokea hoja zenu. Mipango ya Serikali ni mingi na mikubwa sana, tutakwenda kuangalia namna gani ya kufanya ili huduma hii iweze kufika katika kila Jimbo na katika kila Halmashauri. Hilo eneo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo tulisema niweze kulizungumza na katika Mradi wetu wa HEET ambao ni mradi wa vyuo vikuu. Tunafahamu Mheshimiwa Rais ametoa fedha zaidi ya shilingi bilioni 972 kwa ajili ya kuongeza au kuboresha mazingira ya vyuo vikuu nchini. Fedha hizi zitakwenda kutumika katika maeneo makubwa matatu. Eneo la kwanza ni kwenda kujenga miundombinu katika vyuo vikuu hivi vilivyopo lakini vilevile kwenda kujenga kampasi nyingine mpya.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni kufundisha walimu, wahadhiri mbalimbali ili kuwaongezea ubora. Tumezungumza hapa Profesa Ndakidemi amezungumza, Profesa Muhongo saa hizi ametoka kuzungumza kwamba ubora wa vyuo vyetu, hatuwezi kuwa na vyuo bora bila kuwa na mazingira bora. Kwa hiyo eneo la kwanza tunakwenda kujenga miundombinu lakini eneo la pili tunakwenda kufundisha wahadhiri wetu, eneo la tatu tuhakikishe kwamba ni lazima tuwe na vifaa vya kujifunzia na kufundishia. Kwa hiyo, fedha hii tunakwenda kuitumia zaidi ya asilimia 75 itakwenda kwenye hizo infrastructures.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alitoa maelekezo ya namna gani tunaweza tukatumia fedha hii na alielekeza kwamba tusogeze huduma za elimu ya juu karibu na wananchi. Kwa mantiki hiyo, taasisi ambazo zitanufaika na fedha hizi karibu taasisi 19 na vyuo vikuu karibu 14 lakini na taasisi nyingine mfano, Taasisi yetu ya Elimu ya Juu (TCU) nayo itafaidika na fedha hizi, Bodi ya Mikopo itafaidika, amezungumza hapa Profesa Muhongo. Taasisi yetu ya COSTECH nayo vilevile tunaendelea kuifanyia reform kubwa sana. Fedha hii itakwenda kutumika katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, naomba niitaje Mikoa ile michache ambayo itakayokwenda kunufaika moja kwa moja au tunakwenda kujenga kampasi mpya kabisa katika Mikoa ambayo ilikuwa haina kampasi hizo. Mkoa wa kwanza ni Mkoa wa Katavi, tutakwenda kujenga huko, Mkoa wa pili Mkoa wa Lindi tunakwenda kujenga, Mkoa wa Tanga, Tabora, Ruvuma, Manyara, Shinyanga, Singida, Geita, Kigoma, Kagera, Mwanza, Rukwa na Mkoa wa Simiyu. Mikoa hii yote tunakwenda kufanya kazi, mchakato uko katika hatua za mwisho. Tulianza kwanza na feasibility study wameshafanya procurement ya consultant na sasa tunafanya procurement ya contractors na tayari kazi inakwenda kuanza ndugu zanguni. Kwa hiyo, naomba niwaondoe hofu jambo hili linakwenda kufanyika kwa uaminifu na uadilifu mkubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ni eneo la Wadhibiti Ubora; limezungumzwa sana suala la Wadhibiti Ubora na tunafahamu kwamba kulikuwa na waraka toka mwaka 2014, namna gani wadhibiti ubora wanakwenda kuwa na stahiki zile zao za kawaida lakini vilevile mishahara. Ni kweli waraka ule hatujaweza kuutekeleza kwa kipindi chote hiki lakini niwaondoe hofu, Mwezi Aprili mwaka huu tulipeleka muundo mpya wa Wizara ambao umeingiza sasa hawa Wadhibiti Ubora kama viongozi na Mheshimiwa Rais tayari amesharidhia waraka ule toka mwezi wa nne mwaka huu na ifikapo mwezi wa saba, Wadhibiti Ubora wale wote wanakwenda sasa kuwa katika zile kada za uongozi wanaweza sasa wakalipwa zile stahiki kadiri mlivyoshauri tutakwenda kufanya hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la tatu ambalo liliambatana na hilo la wadhibiti ubora ni mazingira yao ya kufanyiakazi, imezungumzwa hapa kwamba katika ukaguzi wa taasisi zetu za shule ni asilimia chache sana kama 26 tu ndiyo ambayo imeweza kukaguliwa. Niwaondoe hofu Serikali imeshafanya makubwa sana kwa upande wa Wadhibiti Ubora. Miongoni mwa mambo ambayo tayari yameshafanyika na Serikali ni ujenzi wa ofisi mpya za Wadhibiti Ubora 160 lakini tumefanya ukarabati wa ofisi za Wadhibiti Ubora 31 lakini vile vile tumenunua magari 119 na kusambaza kwenye Halmashauri pamoja na Wadhibiti Ubora katika Kanda pamoja na Mikoa mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hiyo tumeweza kufanya ununuzi wa kompyuta 195 zile kompyuta za mezani, lakini tumenunua laptop 1,082. Sambamba na hiyo tumesambaza vile vishikwambi ambavyo vilitumika. Vile vilivyogaiwa walimu vilevile wadhibiti ubora wamegawiwa. Lengo kuu hapa la Serikali ni kuhakikisha kwamba tunatengeneza mazingira wezeshi ili wenzetu wadhibiti ubora waweze kufanya kazi yao katika mazingira mazuri na salama kwa sababu ndiyo jicho letu kule la kuangalia elimu ya vijana wetu.

Mheshimiwa Spika, eneo jingine ambalo ningependa labda nilifafanue kidogo ni kwenye eneo la lishe. Nalo vilevile limezungumzwa sana, mnakumbuka tulitoa Waraka wa Elimu Na. 3 wa mwaka 2016 ambao ulikuwa unaeleza wazi namna gani jamii itashirikishwa kwenye suala la kutoa lishe mashuleni. Vilevile tulitoa mwongozo wa mwaka 2022 wa namna gani vile vile jamii itahusishwa.

Mheshimiwa Spika, tumepata malalamiko hapa uchangiaji ule unatofautiana kutoka eneo moja na eneo jingine. Tutakwenda kufanya marekebisho katika eneo hilo ili kuhakikisha kwamba vijana wetu wanapokuwa shuleni wanaweza kupata lishe ambayo itakayowawezesha kujifunza katika mazingira ambayo ni salama.

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsanteni kwa kunisikiliza. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, nami nashukuru kwa kupata fursa hii ya kuweza kuchangia hoja ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu aliyoitoa hapa Bungeni wiki iliyopita.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia tumepokea hoja, mapendekezo na ushauri karibu katika maeneo makubwa manane. Tunaomba tu niwashukuru Waheshimiwa Wabunge kwa hoja zile na kama Wizara kama Serikali, tumezipokea na tutakwenda kuzifanyia kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, naomba tu nitoe ufafanuzi kwenye baadhi ya maeneo machache ambayo tungependa kutoa ufafanuzi mbele ya Bunge lako Tukufu. Eneo la kwanza ni kwenye mapitio ya mitaala yetu ni sera pamoja na sheria, naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu kwamba mchakato huu wa kufanya maboresho kwenye mitaala pamoja na sheria yetu unaendelea vizuri, tunataraji mpaka kufika mwaka 2023 mwishoni nadhani tutakuwa tumekamilisha ili kuweza kupata mtaala ambao ninyi Waheshimiwa Wabunge mnadhani ndiyo ambao unaweza kusaidia Taifa letu.

Kwa hiyo mchakato huo unaendelea vizuri na niwaondoe wasiwasi, kwa namna moja au nyingine tutaendelea kushirikiana nanyi kuhakikisha mawazo pamoja na ushauri wenu unaweza kuzingatiwa katika mitaala hii mipya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee kabisa niombe kuchukua hoja ya Mheshimiwa Dkt. Charles Kimei ambae alizungumzia suala la upungufu wa wafanyakazi au wa walimu katika vyuo vyetu vya ufundi. Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Kimei Waziri wa Utumishi jana ametangaza nafasi mbalimbali za ajira na miongoni mwa nafasi hizo zaidi ya nafasi 2,035 tumepewa sisi Wizara ya Elimu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nikuhakikishie tu Mheshimiwa Kimei na Bunge lako Tukufu kwamba katika maeneo ambayo tutakwenda kuyafanyia kazi ni kuhakikisha kwamba tunakwenda kupunguza upungufu wa Walimu katika vyuo vyetu vya ufundi lakini Wahadhiri katika vyuo vyetu vikuu pamoja na Walimu katika vyuo vyetu vya FDC na maeneo mengine. Kwa hiyo, Mheshimiwa Kimei jambo hili tunakwenda kulizingatia kwa ukaribu kabisa kuhakikisha kwamba upungufu huu tunakwenda kuupunguza kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la pili; Mheshimiwa Shigongo amezungumzia habari ya uanzishwaji wa Mfuko wa Ubunifu (National Innovation Fund), napenda kumpa taarifa Mheshimiwa Shigongo kwamba mwaka 1995 Serikali kupitia COSTECH ilianzisha mfuko huu wawabunifu ambao ulikuwa unaitwa MTUSATE. Kwa hiyo, jambo hili tayari Serikali imeshalifanyia kazi na kila mwaka Serikali imekuwa ikitenga fedha kwa ajili ya kuwaendeleza wabunifu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 zaidi ya Shilingi Bilioni 3.5 zilitengwa kwa ajili ya mfuko huu lakini kwa mwaka 2022/2023 tumekwenda kutenga zaidi ya Bilioni Tisa kwa ajili ya kuuboresha na kuusimamia mfuko huu ili bunifu zetu zilete tija na kutoa majawabu katika changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho alizungumza Mheshimiwa Kishimba suala la kuwahusisha Askari katika usimamizi wa mitihani. Naomba kulitaarifu Bunge lako Tukufu katika taratibu zetu za mitihani hasa ile mitihani ya Shule za Msingi pamoja na Sekondari tuna Kamati zetu za Mitihani za Taifa, Kamati za Mitihani za Mikoa pamoja na Kamati za Mitihani zile za Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili la Halmashauri huwa tunawahusisha Askari katika ulinzi wa mitihani hii la siyo usimamizi wa mitihani kule darasani.

Mheshimiwa Spika, ifahamike tu mtihani wa Darasa la Saba kwa ujumla wake unagharimu zaidi ya Shilingi Bilioni 38.6 sasa tukisema tu kwamba tuuache ule mtihani uende ukafanyike katika mazingira ambayo siyo ya usalama, patakapotokea uvujaji wowote wa mtihani tafsiri yake ni kwamba Taifa linakwenda kuingia hasara ya zaidi ya Shilingi Bilioni 38.6. Kwa hiyo, Askari hawa tumekuwa tukiwahusisha kwenye usafirishaji wa mitihani kutoka katika Mikoa kwenda Halmashauri lakini kutoka Halmashauri kwenda katika center ambazo mitihani inafanyika lakini siyo kwamba Askari anaingia katika chumba cha mtihani na kujihusisha moja kwa moja katika usimamizi wa mtihani. Kwa hiyo, Askari wale wapo katika muktadha wa kuhakikisha kwamba usalama wa mitihani wakati inahifadhiwa lakini usalama wa mitihani wakati inafanyika unaenda sawa sawa ili kutoliingiza Taifa kwenye hasara hii kubwa.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho amezungumza mzungumzaji wa mwisho hapa, amezungumza suala la uwekezaji katika elimu na sisi Serikali yetu imewekeza katika eneo hili la elimu, pia amezungumza suala la scholarship na vitu vingine hili tutakwenda kuliona katika bajeti yetu ya mwaka 2022/2023 kwamba tumetoa kipaumbele kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba tunapata scholarship kwa ajili ya vijana wetu kwenda kupata umahiri na utalaam nje ya Taifa letu.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa ufupi tu nilikuwa naomba kutoa ufafanuzi katika maeneo hayo, naomba kuwasilisha na naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)