Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Questions to the Prime Minister from Hon. Iddi Kassim Iddi (3 total)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tunatambua kwamba Serikali yetu ilizuia kabisa usafirishwaji wa makinikia nje ya nchi na kwa sasa tumeshuhudia makontena ya makinikia yakisafirishwa kupitia barabara ya Bulyanhulu – Kahama na Bandari yetu ya Dar es salaam hivyo kupelekea taharuki kwa Watanzania na kwa wananchi wa Jimbo la Msalala. Nini sasa kauli ya Serikali juu ya jambo hili? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nami nimeona pia kwenye mitandao watu wakionesha kwamba wanaona makontena ya makinikia yakisafirishwa kwenda nje. Nataka niwakumbushe Watanzania kwenye hili kwamba mwaka 2017/2018 tulizuia usafirishaji wa makinikia kwenda nje ya nchi kwa sababu yalikuwa hayajafuata utaratibu lakini pia kulikuwa na udanganyifu mkubwa. Tulipozuia makontena zaidi ya 300/400 yaliyokuwa bandarini yalikaa pale mpaka tulipoweka utaratibu. Utaratibu uliowekwa na Serikali kwanza kuwatambua ni nani wanasafirisha makinikia kwenda nje na ni nani wametoa vibali hivyo kwenda nje na tukazuia kabisa tukaanza utaratibu mpya.

Mheshimiwa Spika, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano alilisimamia na kwa kuunda timu iliyofanya uhakiki wa sekta yote ya madini ikiwemo na eneo hili la usafirishaji mchanga ambalo kwa kweli tulikuwa tunaibiwa kwa kiasi kikubwa. Ufumbuzi wa ile timu ni kuanzisha kampuni ya Watanzania kwa ushirikiano na makampuni ya nje yaliyopo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunayo kampuni inaitwa Twiga Minerals ambayo ni ya Watanzania kwa maana ya Serikali ambayo imeingia ubia na hao wachimbaji wakubwa wa madini kwenye mgodi kama ule wa kwako Mheshimiwa Mbunge wa Bulyanhulu lakini wa pale Kahama Mjini Buzwagi na kule Tarime North Mara. Migodi hii mitatu chini ya Barrick tumetengeneza kampuni ya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwanza wataalam baada ya kuchimba tunapitia kujua aina zote za madini. Mwanzo tuliambiwa madini yaliyopo pale ni ya aina moja tu dhahabu lakini kumbe kule ndani baada ya ukaguzi na uchunguzi wa wataalam tumegundua tuna aina tano za madini. Kwa hiyo, leo hii kupitia Kampuni yetu ya Serikali, inauza madini ya aina zote 5 siyo moja kama zamani. Mbili; tukishapata ule udongo na ukaguzi huo na kugundua aina zote, tunayauza hapahapa ndani ya nchi, sio nje ya nchi. Makontena yote yanayosafirishwa tayari yameshauzwa, Serikali imeshapata fedha yake na fedha imeshahifadhiwa kwenye akaunti zetu kwa hiyo Watanzania hatupati hasara. Hatua inayofuata mnunuzi anakuwa huru kuyapeleka anakotaka na ndio hayo ambayo yanaonekana kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Watanzania kuyaona makontena yakipita na hofu ya awali, nataka niwaondolee kuwa makontena hayo yameshauzwa tayari na huyo ni mnunuzi. Kwa hiyo, waondoe mashaka juu ya usafirishaji wa makontena hayo yenye makinikia kwa sababu Serikali iko makini sana. Inayo timu palepale kwenye mgodi ya kuhakiki lakini pia ya mauzo na kuhakikisha fedha inalipwa na hakuna kontena linatoka nchini bila kuuzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeweka timu pale bandarini kuhakikisha kwamba kila kontena la makinikia linaloingia pale lina nyaraka zote baada ya kufanya mauzo hukohuko kwenye mgodi, kwa hiyo, hakuna kontena linaibiwa. Kwa hiyo, Watanzania muondoe mashaka, Serikali ipo makini, watu wetu tuliowaweka kwenye maeneo haya kuhakiki kuwepo kwa nyaraka zote za kuuza makinikia hayo zipo makini na kwa kweli tunaingiza fedha za kutosha; sina takwimu za kutosha lakini tuna fedha ya kutosha kwa sasa. Mheshimiwa Waziri wa Madini alipokuwa anawasilisha bajeti yake hapa alitoa ufafanuzi na kuonesha namna ambavyo kwenye madini tumepata fedha kiasi kikubwa sana. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kumekuwepo na ongezeko la bei za bidhaa mbalimbali nchini kote, lakini hasa Mkoa wa Shinyanga, Wilaya ya Kahama, Jimbo la Msalala na hususan bidhaa hizo ni mafuta ya kula, sabuni, lakini pia vifaa vya ujenzi kama nondo, simenti. Ni nini sasa kauli ya Serikali juu ya ongezeko au mfumuko wa bei katika bidhaa hizi mbalimbali? Ahsante. (Makofi)
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza siku za karibuni kupanda kwa bei kwa baadhi ya bidhaa zinazozalishwa hapa nchini. Upandaji wa bei hizi wakati mwingine ni wa makusudi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara ambao sio waaminifu, lakini pia, upatikanaji wa malighafi. Viwanda vyote ambavyo vinazalisha hapa nchini vingi miongoni mwake vinategemea malighafi kutoka hapa nchini na malighafi zipo.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka siku tatu, nne zilizopita, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, amezungumza na Taifa kwa kuwaambia kwamba, uko mkakati wa baadhi ya wafanyabiashara waovu wasiokuwa na nia njema wa kupandisha bidhaa kwa makusudi tu; moja, kwanza wanazalisha kidogo sana ili kutengeneza upungufu mtaani ili bei ziweze kupanda. Mbili, kumekuwa na utamaduni sasa wa baadhi ya wafanyabiashara waovu kukaa pamoja na kujadili tu bei ziweje na kusababisha mfumuko wa bei. Serikali tumeligundua hilo na ndio kwa sababu, Waziri Dkt. Kijaji, ametoka hadharani kutueleza mkakati wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono kauli yake, lakini pia, natoa agizo kwa wafanyabiashara kuacha tabia hiyo ovu inayosababisha jamii kushindwa kupata bidhaa kwa gharama nafuu kwa sababu, wakati tunawekeana mikataba na wakati tunajenga mazingira rahisi ya uwekezaji nchini, lengo la kwanza kubwa ilikuwa ni kupata bidhaa kwa wingi, kwa bei nafuu, lakini pia zipatikane wakati wote, sasa wengine wanaanza kukiuka masharti yetu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ametoa ultimatum kwao, nami narudia tena, hatutasita kuchukua hatua kwa wafanyabiashara ambao wanaweka mkakati tu wa kutaka kusumbua jamii kwa kununua bidhaa kwa bei ya juu bila sababu yoyote, kwa sababu, bidhaa tunazo, malighafi tunazo na viwanda vipo, uboreshaji ndani ya Serikali wa uwekezaji tumeufanya kwa kiasi kikubwa na kila siku tunakutana nao na wanaeleza namna ambavyo tungependa Serikali iwe na sisi Serikali tunafanya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili ambalo Mheshimiwa amelieleza, Serikali itaendelea kuchukua hatua kali na tutasimamia upandaji wa bidhaa hizi usiende kupanda mara zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niiagize taasisi yetu inaitwa FCC, ambayo inasimamia haki za wafanyabiashara katika kufanya biashara, ihakikishe inafanya ukaguzi wa kina kila bidhaa zinazozalishwa na mauzo yao, walinganishe na uzalishaji wao, uwezo wa kiwanda kwa mwaka, tuone kama je, wanazalisha kwa kiwango kilekile tulichokubaliana au wamepunguza uzalishaji kutengeneza upungufu? Pia tujue kwa nini wanapandisha bei, kati ya kiwanda na kiwanda bei zinatofautiana? Hili nalo tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niahidi kwamba, tutalifanyia kazi kupitia taasisi zetu za ndani ya Serikali, kama alivyoahidi Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekuwepo na ongezeko la mizani za kupimia mizigo ya magari nchini kote na hivyo kuongeza idadi kubwa ya watumishi katika mizani hizo, ambao kimsingi hawa mikataba ya kudumu. Sasa ukosekanaji wa mikataba ya kudumu inasababisha kukosekana kwa haki yao msingi kukopa. Nini kauli ya Serikali na hasa ukizingatia ajira hizi mpya watumishi kupata ajira za kuduma?
WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeongeza huduma za upimaji wa uzito wa magari nchini ambako tunavyo vituo maalum vilivyojengwa, lakini pia tunazo mizani zinazotembea kwa lengo la kuhakiki uzito wa magari ili yanapopita kwenye barabara zetu tusipate uharibifu mkubwa, kwa kuongeza mizani pia tumeongeza watumishi waliopo chini ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, sasa watumishi hawa ni sehemu ya watumishi wote ambao wanapata mikataba yao.

Mheshimiwa Spika, iko mikataba ya muda mfupi, iko mikataba ya kudumu na tunafanya hilo ili kuwezesha pia watumishi hao kuwa na stahiki zao za kimsingi. Sasa ni lini tutaweza kuimarisha mikataba hiyo ili wapate haki zao za kudumu pamoja na stahiki zingine ikiwemo mikopo na haki nyingine, hili linategemea pia na nafasi za ajira Serikali na nafasi ambazo zinapewa sekta ya ujenzi kwenye mizani ili kuweza kuwaajiri moja kwa moja watumishi hawa.

Mheshimiwa Spika, ninalichukua hilo na Waziri wa Uchukuzi yuko hapa anasikia, kwa hiyo, ni jukumu sasa la kuratibu vizuri watumishi wote wanaofanya kazi kwenye mizani wenye mikataba ya muda mfupi kuona kama wanazo sifa za kupata ajira za kudumu ili wapate mikata ya kudumu na hatimaye haki zao ziweze kusaidiwa. (Makofi)