Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Iddi Kassim Iddi (29 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia uhai na afya iliyo bora, lakini pia nikushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii leo ili niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama katika Bunge lako Tukufu nianze kwa kuwashukuru wananchi wangu wa Jimbo la Msalala kwa kunipatia imani kubwa hii ya kuweza kuwawakilisha katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii tunajadili hotuba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, niseme sisi kama Wanajimbo la Msalala, hotuba hii imeleta mapinduzi makubwa sana katika Jimbo langu la Msalala. Niliarifu Bunge lako Tukufu hili kwenye ukurasa wa 37, lakini pia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Rais ya 2020, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli katika Jimbo la Msalala ameweza kutupatia miradi mikubwa kabisa ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais ametupatia mradi mkubwa wenye zaidi ya bilioni 13 ambao ni mradi wa maji unaotoka Magu kuja Ilogi. Hata hivyo, hajaishia hapo Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ametupatia mradi mkubwa kabisa wa maji unaotoka Kagongwa kwenda Isaka unaogharimu kiasi cha bilioni 23. Pia hajaishia hapo, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameweza kutupatia mradi mwingine wa maji ambao unatoka Nduku Mtobo kwenda Busangi, ambao unagharimu kiasi cha shilingi bilioni nne nani kama Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tumeona azma yake ya kuunganisha mikoa kwa mikoa, wilaya kwa wilaya. Katika Jimbo langu la Msalala, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ameweza kutupatia barabara mbili zenye kiwango cha Lami, barabara hizi ni barabara inayotoka Solwa kuja kupita Kata ya Ngaya na Kata ya Bulinge kuja Kahama lakini pia ametupatia barabara nyingine inayotoka Bulyanhulu kuja Segese mpaka Kahama. Naiomba Wizara ya Ujenzi iweze kuona namna gani inaweza kuanza utekelezaji wa barabara hizi mapema iwezekanavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala nzima la afya, niseme tu mbele yako Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa sisi Wanabulyanhulu alianza kupambana juu ya kupitia mikataba upya ya madini na mikataba hiyo sisi kama Wanamsalala tumeweza kunufaika pakubwa sana na mikataba hii. Leo hii ninapozungumza tunapokea fedha za CSR. Nimwombe kaka yangu Mheshimiwa Doto Biteko, Waziri wa Madini aweze kufanya ziara na kuona namna gani sasa Wanamsalala tunaweza kunufaika na fedha hizi za CSR.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na ucheleweshwaji wa miradi mbalimbali inayopangwa kwa ajili ya kutekelezwa na watu hawa wa mgodi zinazotolewa na fedha za CSR. Nimwombe kaka yangu Mheshimiwa Doto aweze kufika katika Jimbo langu la Msalala ili tuweze kufanya kikao na watu hawa tuone namna gani wanaweza kutekeleza miradi hii ya CSR ili iweze kuleta tija kwa wananchi wa Jimbo la Msalala.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii hotuba ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli imeweza kutufanya Jimbo la Msalala kuhama kutoka uchumi wa chini na kuhamia uchumi wa kati. Ninavyozungumza hapa tuna vituo vinne vya afya katika Jimbo langu la Msalala, lakini pia tunaenda kujenga kituo kingine kwa fedha zetu za ndani za jimbo, tunaenda kujenga kituo cha afya katika Kata ya Isaka. Niiombe TAMISEMI na Waziri Mheshimiwa Jafo, kaka yangu aweze kutusaidia kutupatia vifaa tiba ili kituo cha afya kinachokamilika kiweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi letu sio hilo tu, lakini tumekuwa na uhaba wa watumishi katika sekta ya afya katika Jimbo la Msalala; nimwombe Mheshimiwa Jafo aweze kutuangalia kwa jicho la huruma Wanamsalala, tuna uhaba wa Walimu pia, naomba ndugu yangu atusaidie katika suala hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri Mkuu juu ya kauli yake ya kuhakikisha kwamba tunaenda kuongeza madarasa katika nchi nzima. Katika Jimbo langu la Msalala napenda nimhakikishie Mheshimiwa Waziri Mkuu tulilipokea wazo lake hilo na maagizo yake hayo kwa kutekeleza ujenzi wa madarasa na tumeweza kuongeza madarasa katika kila kata mawili. nami kama Mheshimiwa Mbunge, nimhakikishie Mheshimiwa Waziri Mkuu nilitoa lori la cement kuhakikisha kwamba naunga juhudi za ujenzi wa madarasa hayo. Kwa sasa tunavyozungumza tuko katika hatua nzuri na baadhi ya shule tayari madarasa hayo yameanza kutumika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nije kwenye suala la ajira..

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Muda umeisha Mheshimiwa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia fursa hii ili kuchangia leo Mpango wa Tatu. Kwanza kabisa nianze kuwashukuru wananchi wa Jimbo la Msalala. Lakini pia leo nitachangia katika maeneo matatu; eneo la kwanza nitachangia eneo la kilimo, na eneo la pili nitachangia eneo la madini na biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi kubwa aliyoifanya katika Taifa hili. Kila mmoja ni shahidi wa mambo ambayo kimsingi Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ametufanyia sisi Watanzania. Tuna haja kubwa ya kumpongeza Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo langu la Msalala limegawanyika katika maeneo mawili; eneo la kwanza ni kilimo. Asilimia 50 ya jimbo langu ni kata ambazo kimsingi zinafanya shughuli za kilimo, lakini kumekuwa na tatizo katika suala zima la utoaji wa vibali ambacho kitawaruhusu wakulima hawa baada ya kupata mazao mengi waweze kusafirisha kwenda kuuza nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu uliowekwa na Wizara ya Kilimo ni kuhakikisha kwamba wakulima hawa wanaweza kuomba kibali kwa kutumia njia ya mtandao. Ni ukweli usiopingika kwamba katika maeneo yetu, hasa ukizingatia maeneo ya Kata za Mwaluguru na Mwanase, ni maeneo ambayo hayana mawasiliano. Nimwombe Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo na Waziri wa Kilimo waweze kuona namna gani wanakwenda kushirikiana na Waziri wa Mawasiliano ili kuweza kuhamisha mawasiliano ambayo yatawafanya basi sasa wananchi hawa, wakulima hawa, waweze kupata huduma ya mtandao ili waweze ku-apply kibali hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe sasa Wizara iweze kubadilisha utaratibu huu wa wananchi kuomba kibali kwa kupitia njia ya mtandao, kwani tunaamini kuwa wananchi wengi hawawezi kuingia kwenye mtandao na kujaza taarifa za kuomba kibali hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba kwa sasa kumeibuka tabia ya kwamba kila maeneo wanaweza kuanzisha mazao mbalimbali ikiwemo korosho na mengine. Niseme tu kwamba sisi wananchi wa Shinyanga ni wakulima wa zao la pamba, lakini kumeibuka tabia ya sasa hawa Maafisa Kilimo kuanza kutuletea mazao mapya. Niombe Waziri wa Kilimo yuko hapo, Naibu Waziri wa Kilimo yuko hapo, waone namna gani sasa wanaweza wakahakikisha kwamba wanatu-support ili tuweze kwenda kwenye kilimo cha pamba kwa kutupatia fedha na mitaji na matrekta yetu yaingie kwenye zao la kilimo cha pamba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala zima la madini. Jimbo langu la Msalala ni jimbo ambalo kimsingi lina Mgodi mkubwa wa Bulyanhulu. Nimwombe Waziri wa Madini yuko hapo, Mheshimiwa Doto Biteko, kwanza niwapongeze kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuhakikisha ya kwamba wameweka makubaliano na Kampuni ya Twiga. Ni ukweli usiopingika kwamba wanasimamia vizuri shughuli hizi za madini na usimamiaji wa utoroshaji wa madini. Hata hivyo, nimwambie tu Mheshimiwa Waziri kwamba kampuni hii kwa sasa nadhani imeanza kuja na mfumo mwingine ambao kimsingi kama Taifa tunakosa mapato lakini kama halmashauri tunapoteza fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kampuni hii imeanzisha kampuni mbili ambayo moja iko Marekani inaitwa TSL. Uwepo wa kampuni hii Marekani kama Taifa tunapoteza mapato. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, kampuni hii ipo USA maana yake kazi kubwa ya kampuni hii ni kutangaza tenda tu na zabuni mbalimbali katika makampuni makubwa makubwa. Kwa nini kampuni hii isweze kurudi hapa nchini, Makao Makuu yake yakawa Dar es Salaam ili kama nchi tuweze kupata mapato?

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, Kampuni hii imeanzisha mtoto wa kampuni ambayo inaitwa TSR Service, iko Dar es Salaam. Uwepo wa Kampuni hii Dar es Salaam inatufanya Halmashauri kupoteza zaidi ya shilingi bilioni 20 fedha za Service Levy. Namwomba Mheshimiwa Waziri, kwa kushirikiana yeye na Waziri wa Viwanda waone ni namna gani sasa wanaweza kuzishauri kampuni hizi ziweze kuja kuwekeza na kuanzisha ofisi zao katika maeneo ya kazi hususan Bulyanhulu. Uwepo wa kampuni hii Dar es Salaam unasababisha ukosefu wa ajira kwa wananchi wetu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MBUNGE FULANI: Unga mkono hoja.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. IDDI KASSIM IDDI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami kwa kunipatia leo nafasi hii ya kuchangia. Kwa niaba ya wanananchi wa Jimbo la Msalala naomba niipongeze Serikali kwa mambo makubwa na mazito kabisa ambayo yamefanyika ndani ya miaka mitano iliyopita na ambayo kwa sasa yanaendelea kufanyika kwa Awamu hii ya Sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo tumesomewa mpango hapa na hotuba ya Waziri Mkuu kwa ajili ya bajeti ya Waziri Mkuu. Hotuba hii ya bajeti ya Waziri Mkuu ni hotuba iliyoshiba kweli kweli; imeeleza wapi tumetoka na inatuelekeza wapi tunaenda. Niseme kwamba katika hotuba hii ya bajeti Waziri Mkuu ameelezea mambo mengi na nijikite kuelezea mambo machache.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuelezea mradi wa Julius Nyerere. Mradi huu wa Julius Nyerere ni mradi muhimu sana na niseme tu kwa niaba ya wananchi wa Msalala, tunaunga mkono Serikali ili mradi huu uende ukatekelezwe na ukamilike. Kwa hiyo, tunafahamu the cheapest source of energy kwenye nchi hii ni umeme unaotokana na maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia gharama ya sasa ya umeme, wananchi wetu wanalia huko; unit moja kwa sasa ni shilingi 100/=, lakini ukiangalia manufaa ya mradi huu utakapokamilika, uzalishaji wa unit moja katika mradi huu wanaenda kutumia kiasi cha shilingi 36 kuzalisha unit moja. Maana yake nini? Ni kwamba itaenda kushusha gharama ya uzalishaji kwenye viwanda na pia itashusha gharama ya unit kwa wanananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme, japo mradi huu utaenda kukamilika, niipongeze Wizara ya Nishati, inafanya kazi kubwa. Katika Jimbo langu la Msalala ni ukweli usiopingika kwamba watu wa Nishati wanafanya kazi kubwa, lakini kuna baadhi ya maeneo umeme huu haujafika. Wananchi wa Msalala tunapoona mtu anasimama na kuupinga mradi huu, tunashikwa na hasira kwa sababu Jimbo la Msalala lina Kata 18 na Kata zaidi ya 12 hazina umeme. Kwa hiyo, matarajio yetu ni kwamba mradi huu wa REA III ambao kimsingi utaenda kukamilika, ni kwamba baada ya mradi huu wa Mwalimu Nyerere kukamilika tutakuwa na umeme wa uhakika lakini pia nasi wananchi wa Jimbo la Msalala tutanufaika na nishati hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala la kilimo. Katika Kata 10 katika Jimbo langu la Msalala ni wakulima wa mpunga. Kuwepo na ukamilishaji wa mradi huu na uwekwaji wa umeme katika Kata zetu hizi utachochea uchumi kwa wakulima. Maana yake nini? Wakulima wataweza sasa kuchakata na kuongeza dhamani ya mazao hayo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye suala la madini. Nimeona hapa imeelezewa na ninaipongeza Wizara imefanya kazi nzuri sana kwenye Sekta ya Madini. Namwomba Mheshimiwa Waziri Dotto hapa, sisi tunaotoka katika maeneo ya migodi, Mheshimiwa Bonnah Kaluwa amezungumza hapa, kuna masuala ya fidia ambayo kimsingi imekuwa ni tatizo katika maeneo yetu haya.

SPIKA: Mheshimiwa, anaitwa Bonnah Kamoli.

MHE. IDDI KASSIM IDDI: Mheshimiwa Bonnah Kamoli.

SPIKA: Eeeh! (Makofi/Kicheko)

MHE. IDDI KASSIM IDDI: Mheshimiwa Spika, kuna tatizo la fidia kwenye eneo langu. Tunatambua ya kwamba kuna mgodi umeanzishwa pale katika eneo letu Kata ya Bulyanhulu ambao ni mgodi wa Bulyanhulu. Baada ya hao watu kuanzisha mradi pale kuna watu mpaka leo toka mwaka 1966 hawajalipwa fidia ya ardhi yao. Naiomba Wizara na Serikali kuhakikisha ya kwamba tunamaliza tatizo hili, kwani ni la muda mrefu sana. Tatizo hili limedumu toka Mheshimiwa Rais Mwinyi akiwa bado ni Rais.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba Wizara kwamba sasa tuhakikishe tunatatua tatizo hili la mgogoro na fidia kwa wananchi hao wa Kata ya Bulyanhulu.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo, maslahi ya wafanyakazi. Bado kuna wafanyakazi wanadai. Naomba sasa Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri wameshaanza kulifanyia kazi, waharakishe kuhakikisha kwamba wafanyakazi wale wanapata stahiki zao mapema ili waweze kujikita kwenye shughuli za uchumi na kutumia fedha hizo katika mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumzie suala la maji. Tuna miradi ya maji katika Jimbo langu la Msalala. Ni kazi nzuri inafanywa na kaka yangu Aweso, lakini namwomba Mheshimiwa Aweso aweze kuharakisha mradi wa maji unaotoka Mangu mpaka Ilogi uweze kukamilika. Baada kukamilika sasa waanze usambazaji wa maji mara moja katika Kata ya Ikinda, Kata ya Runguya na Kata ya Segese ili wananchi wale nao waweze kufaidika na huduma hii ya maji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la barabara limekuwa ni mtihani. Wabunge wengi wanalia hapa kuhusu suala la TARURA, lakini mimi naweza nikasema ni jimbo langu la Msalala ni jimbo ambalo lina miundombinu mibovu sana katika. Leo hii tunapozungumza hapa, Ilani ya Chama cha Mapinduzi na Hayati Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli wakati wa kampeni, tuliahidiwa kupata barabara mbili zenye kiwango cha lami. Kuna barabara inayotoka Geita - Bukori -Kata ya Bulyanhulu – Kahama. Barabara hii tuliahidiwa kujengwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia naomba niikumbushe Wizara kwamba wakati Serikali inaingia makubaliano na mgodi huu wa Twiga, moja ya makubaliono ambayo walikaa wakakubaliana ni kuhakikisha kwamba wanatenga kiasi cha dola milioni 40 ili waweze kukamilisha barabara hii kwa kiwango cha lami. Fedha hizi zipo, naiomba Wizara husika iweze kuona ni namna gani sasa wanaenda kukaa na kuzungumza fedha hizi zipelekwe ujenzi ili barabara hii ianze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Spika, hivyo hivyo, tuna barabara nyingine ambayo inatoka Solwa inakuja Bulige inaenda Ngaya na Kahama. Barabara hii pia imeahidiwa kwa kiwango cha lami. Naendelea kuomba Wizara ione namna gani basi inaweza kuanza ujenzi wa barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna barabara moja ambayo ni ndefu sana ina zaidi ya kilometa 85. Barabara hii inaunganisha Makao Makuu na Jimbo la Solwa. Naomba Wizara ya Ujenzi waone namna gani basi wanaweza kuanza mchakato wa kuihamisha barabara hii kutoka TARURA iende TANROADS ili ingie kwenye matengenezo ya kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kuishia hapo, niseme kwamba naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Madini
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipatia nafasi hii. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala, naomba na mimi nichangie katika hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Madini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nianze kwa kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa inayoendelea kuifanya, lakini pia ni ukweli usiopingika kwamba tunaona kabisa Wizara ya Madini inavyofanya kazi kubwa katika kuhakikisha kwamba inachangia pato la uchumi wa nchi yetu katika kuimarisha mambo mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kuipongeza Wizara ya Madini kwa kuanzisha masoko mbalimbali na hasa katika Jimbo langu la Msalala, tumeona Waziri wa Madini ameweza kutoa maelekezo na Serikali imeweza kuanzisha masoko ya madini katika Kata za Bulyanhulu na Segese. Niombe tu Mheshimiwa Waziri baada ya kikao hiki cha Bunge basi uweze kutembelea ili kusikiliza changamoto za wachimbaji wadogo katika maeneo hayo, hususan Kakola, Bulyanhulu na Kata ya Segese.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona hotuba ya bajeti ilivyoelezea juu ya namna gani Wizara imejipanga katika kuhakikisha kwamba inakwenda kuwawezesha wachimbaji wadogowadogo. Niipongeze Wizara inafanya jitihada kubwa katika kuhakikisha kwamba inawawezesha wachimbaji wadogowadogo, lakini ni ukweli usiopingika kwamba bado kuna changamoto ndogondogo ambazo kimsingi niombe Wizara iweze kuzishughulikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii STAMICO wameonesha mkakati wao kwamba wanakwenda kujipanga katika kusimamia na kuwawezesha wachimbaji wadogo. Hata hivyo, katika maeneo yetu wachimbaji hawa wamekuwa wakinyanyasika sana kwa kukosa mitaji au mikopo kutoka katika taasisi mbalimbali. Niiombe Wizara iweze kufikiria sasa namna gani wanaweza kuanza kutoa mikopo kwa wachimbaji wadogo ambao ndiyo shokomzoba ya Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ametueleza hapa mchango wa wachimbaji wadogowadogo katika kuchangia uchumi wa pato la Taifa. Ni ukweli usiopingika kuwa hawa watu wanafanya kazi ngumu sana. Naomba nishauri twende tukaweke mkakati kuhakikisha kwamba tunakabiliana na matapeli kwa sababu wamekuwa wengi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri ametueleza hapa namna gani wamefanya jitihada kuwapatia wachimbaji wetu wadogo leseni, niipongeze Wizara katika baadhi ya maeneo yangu hususan Nyangarata na maeneo mengine katika Jimbo la Msalala, Wizara wamefanya hivyo lakini namna gani wanakwenda kutoa leseni hizi lazima tukueleze leo na tutoe ushauri, kwamba watu wanaokwenda kupata leseni katika maeneo haya ni watu ambao kimsingi sio original katika maeneo yale na wengi wao ukiwatafuta unakuta ni madalali. Leo hii unakuta mtu anamiliki shamba, lakini siyo shamba tu ameanzisha uchimbaji na akagundua madini katika maeneo yale, anatoka mtu anakotoka anakuja na leseni kujitambulisha pale na anasema yeye ndiyo mmiliki halali wa maeneo yale. Hii inamnyima haki mchimbaji wetu na tunampa kazi ngumu katika kuhakikisha kwamba anachangia pato la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe Waziri wa Madini wakae kama Wizara waone namna gani wanaweza wakauboresha huu mfumo wa kuomba kwa mtandao (portal). Watu wetu huko vijijini network hakuna Mheshimiwa Waziri inawanyima haki ya wao kumiliki leseni hizi. Niiombe Wizara iweze kuona namna gani wanaweza wakaweka mfumo mzuri ili iweze kuwarahisishia wachimbaji wetu wadogo, hususan wakazi wa Bulyanhulu, Nyangarata, Segese na maeneo mengine katika Jimbo langu la Msalala kuwa na haki hii ya kuweza kupata leseni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niipongeze Serikali, imefanya kazi kubwa kuhakikisha wanaunda ubia kati ya Twiga na Serikali na nipongeze jitihada ambazo zimesemwa. Mimi nizungumzie suala hili katika maeneo mawili; katika local content na fedha za CSR.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Musukuma amesema hapa katika Jimbo lake la Geita wanapewa fedha za CSR kiasi cha shilingi takribani bilioni 10, lakini inasikitisha kuona Jimbo langu la Msalala ambalo tunamiliki Mgodi wa Bulyanhulu, tunapokea fedha za CSR bilioni 2.5 tu na wakati migodi yote ipo Tanzania. Kwa nini Geita wapokee bilioni 10 na sisi tupokee bilioni mbili? Namwomba Mheshimiwa Waziri akimaliza hapa tufanye ziara tuone ni kwa nini kuna tofauti hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mambo yote tunayojadili hapa ni ukweli usiopingika kwamba watumishi wa kwenye Tume ya Madini ni wengi lakini bajeti yao ni ndogo. Ukiangalia watumishi katika Wizara ni wachache lakini bajeti kubwa inakwenda Wizarani na hii inasababisha Tume ya Madini isifanye kazi zake kiuhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, makampuni haya; GGM na makampuni mengine yote, hususan nizungumzie katika Jimbo langu la Msalala, Bulyanhulu pale, kumekuwa na uvunjaji mkubwa wa sheria ya local content. Leo hii tunazungumzia namna gani ya kuwakuza wachimbaji wadogo kutoka katika ngazi ya chini kwenda ngazi ya kati na tuwafanye wachimbaji hao wawe wakubwa lakini ni ukweli usiopingika tunaona kabisa migodi hii wanachangia kwa kiasi kikubwa kuvunja Sheria ya Local Content. Tuna wafanyabiashara wana uwezo wa ku-supply katika migodi yetu hii hawana kazi, kumekuwa na matapeli katikati hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikiwa bado M-NEC nilimsikia Mheshimiwa Waziri akitoa maelekezo katika Mgodi wa GGM waweze kutekeleza sheria hiyo ya local content kuhakikisha kwamba wazawa wanapewa nafasi lakini watu hawa wana kiburi, hawajatekeleza yale aliyowaambia. Watu hawa wana dharau kubwa, nenda kawaeleze kwamba sisi kama wananchi tunaoishi katika maeneo yale ya mgodi tuna-play part kubwa ya kuhakikisha usalama wao na mali zao na ni lazima sasa wakazi tunaoishi katika maeneo yale hususan Bulyanhulu na meneo mengine kama ya Bugarama tunanufaika na migodi hiyo. Kama leo hii hawataweza kutekeleza sheria hii ya local content…

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kassim, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nampa taarifa mzungumzaji kwamba baada ya tamko la Mheshimiwa Naibu Waziri kule GGM kwamba GGM watekeleze local content, walitekeleza kwa kutoa zile kazi kama ku-supply nyanya na vitunguu, zile kazi zenye maslahi zote wanafanya Wazulu.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, napokea taarifa hiyo ya Mheshimiwa Musukuma kwa mikono miwili na sisi Wanamsalala tulishafikisha kilio chetu …

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kassim, inabidi usubiri kwanza nikuite tena ndiyo uzungumze. (Kicheko)

Mheshimiwa Kassim Iddi Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kupokea taarifa hii kwa mikono miwili, lakini unisamehe kwa sababu ya unjuka, nitazoea. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakubaliana asilimia 100 na Mheshimiwa Musukuma. Leo hii makampuni haya ni ukweli usiopingika Mheshimiwa Waziri anafahamu, baada ya kuona Wizara imeweka mifumo ya kudhibiti utoroshaji wa madini sasa wameamua kuja na mfumo mpya kuhakikisha wanatupiga sisi Serikali lakini pia Halmashauri yangu ya Msalala.

Mheshimiwa Naibu Spika, hili nimeshalifikisha kwa Waziri na naomba alishughulikie haraka iwezekanavyo. Tumekuwa wavumilivu sana wananchi wa Bulyankhulu na Msalala. Tunatamani mgodi huu uendelee kuwepo, leo hii tulikuwa tunazungumza kwamba kampuni hizi zimeanzisha kampuni ndogo pale Dar es Salaam, TCL Mheshimiwa Waziri, tumeshalizungumza hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii mama anayelima nyanya katika Jimbo langu hawezi ku-supply nyanya kwenye mgodi mpaka aende Dar es Salaam. Hivyo mnatutoreshea mapato katika Halmashauri yetu. Naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hili haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri suala la barabara, fedha nendeni mkatekeleze haya barabara ianze kupitika. Mimi na wananchi wangu tumekubaliana ikifika mwezi wa Saba barabara haijatengenezwa, fedha hazijatoka, Mheshimiwa Waziri sisi tutaziba barabara, kwa sababu wananchi wangu wanahangaika mno. Tunanufaika vipi na madini haya kama wananchi wetu wanakula vumbi? Kwa hiyo, naomba Wizara ya itekeleze haya ili wananchi wetu waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naunga mkono hoja asilimia mia moja na mbili. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipatia fursa hii nami kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala kuchangia juu ya bajeti hii ya Wizara ya Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitajikita katika maeneo matatu kama muda utaniruhusu, na nianze moja kwa moja kwa kujikita katika suala zima eneo la madini. Lakini nianze kwa kumshukuru Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika Taifa letu la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitachukua nafasi hii kukishukuru Chama changu cha Mapinduzi kwa ajili ya kuniamini mimi na kuwawakilisha wananchi wa Jimbo la Msalala lakini pia kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya. Tumeona Katibu Mkuu na Sekretarieti nzima ikizunguka kwa ajili ya kuinadi na kuisimamia Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nichukue nafasi hii pia kuwapongeza Mawaziri na wafanyakazi wote wa Wizara ya Madini. Pia nimpongeze Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutupatia fedha kiasi cha shilingi 500,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa kilometa Moja barabara ya lami katika Kata ya Bulyanhulu. Kwa hiyo, nimpongeze Mheshimiwa Rais kwa kuona namna gani sasa wananchi wa Bulyanhulu wanasumbuliwa na vumbi na kutupatia kiasi cha shilingi 500,000,000 walau tuweke kilometa moja ya lami katika eneo lile ili tuweze kupunguza vumbi lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze Dada yangu Mheshimiwa Ummy Mwalimu kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Lakini pia niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kutupatia shule moja ya sekondari ambayo tunaenda kuijenga katika Kata ya Ikinda ambayo itapunguza adha ya ukosefu wa shule katika Kata ile ya Ikinda. Lakini niendelee kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais na Wizara kwa kutupatia kiasi cha shilingi 1,000,000,000 kwa ajili ya ujenzi wa hospitali yetu ya wilaya. Hivyo hivyo, nimpongeze Mheshimiwa Rais tena kwa kutupatia kiasi cha shilingi 750,000,000 kwa ajili ya ukamilishaji wa jengo la utawala katika Wilaya yangu ya Msalala. Nimpongeze pia kwa kutupatia kiasi cha shilingi 500,000,000 katika ujenzi wa kituo cha afya kinachoendelea katika Kata ya Isaka. Mambo mengi Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ametutendea katika jimbo langu la Msalala. Hivyo, kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala ninamshukuru na tunamshukuru kwa dhati Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa kututendea wema huu katika Jimbo langu la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende sasa moja kwa moja kuchangia katika Sekta hii ya Madini. Sekta ya Madini kama mnavyofahamu imetembea katika misuko suko mikubwa sana mpaka hapa ilipofikia. Sekta ya Madini imekabiliwa na changamoto nyingi, nimshukuru Waziri wa Madini kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya kuhakikisha kwamba sekta hii ya Madini inasimama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende moja kwa moja kuchangia nimeona hapa kwenye bajeti hii kuna tozo ambayo inaenda kuanzishwa kwa wachimbaji wa madini wadogo wadogo na hii Mheshimiwa Waziri nikuambie ukweli, hii tunayoenda nayo kwa sasa ambayo inawataka wachimbaji wadogo wadogo wenye makusanyo yasiyozidi milioni mia moja kwenda kulipa tozo ambazo zimeorodheshwa hapa. Hii kiukweli tunaenda kuua Sekta hii ya Madini. Sekta ya Madini Mheshimiwa Waziri nikuambie ukweli, Sekta ya Madini kwa sasa tunaona kabisa kwamba Wizara zingine zote, Sekta ya Madini wameiona sasa kama ni Sekta ambayo ya kwenda kukusanya fedha. Sekta ya Madini tunakabiliwa na changamoto nyingi sana hasa za kikodi. Kuna kodi nyingi sana katika Sekta ya Madini na ili Sekta hii iende ikasimame ni lazima tuone namna gani tunaenda kuisaidia sekta hii katika kupunguza gharama na tozo mbalimbali zilizoko hapa.

Mheshimiwa Waziri, leo hii tunakwenda kumwambia mchimbaji mdogo mdogo anapokwenda kuuza madini yake katika soko la dhahabu aende akakatwe tozo ya zuio la ajira. Leo hii tutambue Mheshimiwa Waziri, huyu mchimbaji mdogo mdogo kwanza hana maeneo ya kuchimba ambayo ni rasmi na utaratibu unaotumika kule ni kwamba mtu anayemiliki leseni ni tofauti kabisa na mchimbaji mdogo mdogo anayechimba katika leseni ile. Sasa, baada tu ya huyu mchimbaji mdogo mdogo kuchimba madini yake kunakuwa na migao mingi ambayo kimsingi inaenda kufanyika pale kabla hata ya kwenda sokoni kuuza dhahabu yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wachimbaji wadogo wadogo hawajaajiri watu, wanapochimba mathalani mchimbaji ametoa mifuko 100 kwenye shimo lake, hapo hapo anakatwa mifuko kwa ajili ya mmiliki wa leseni mifuko ishirini na zaidi. Hapo hapo anakatwa kwa ajili ya ulinzi, hapo hapo anakatwa kwa ajili ya wafanyakazi, hapo hapo wanamalizana. Maana yake ni kwamba mtu anapotoka na dhahabu yake mchimbaji mdogo mdogo huyu kwenda sokoni ameshamalizana na mambo mengine yote huku. Unaendaje kumkata tena fedha pale kwenye soko la dhahabu anapouza kwa ajili ya kulipa zuio la ajira? Mheshimiwa Waziri nikuombe hebu nendeni makapitie upya mapendekezo haya mliyoyaleta yanaenda kuua Sekta ya Madini. Sisi kama wachimbaji wadogo wadogo tuko radhi kuhakikisha ya kwamba tunalipa kodi. Lengo la kuanzishwa masoko haya ni kudhibiti utoroshwaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwa kodi hizi zinazoendelea kuwekwa hapa inaenda kufungua tena milango ya kuhakikisha kwamba utoroshaji wa dhahabu unaendelea. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, nenda kapitie upya. Hili suala haliwezekani, wachimbaji wadogo wadogo hawa wasiopitia mauzo ya chini ya milioni 100 hawawezi wakalipa mambo yote hapa, hapa yamewekwa kuna kodi inakatwa asilimia tatu ambayo kodi hii tayari ameshailipa kule mifuko. Imewekwa hapa anatakiwa akatwe kodi ya mapato ya ajira, huyu anamuajiri nani mchimbaji mdogo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe chonde chonde twendeni tuhakikishe ya kwamba tunaenda kuondoa kodi hizi ili kumrahisishia mchimbaji mdogo mdogo. Lakini pia niiombe Wizara badala ya kujikita kuongeza kodi hizi tujikite katika kuhakikisha ya kwamba tunaenda kuwajengea uwezo wachimbaji wetu hawa wadogo wadogo. Leo wachimbaji wadogo wadogo wanahangaika na ukosefu wa mitaji, wanahangaika na ukosefu wa maeneo sahihi ya uchimbaji, tafiti hazitolewi kuwawezesha wachimbaji wadogo wadogo hawa ili waweze kuchimba maeneo sahihi, hazitolewi. Leo hii tunaenda kuongeza kodi tena. Mheshimiwa Waziri nikuombe, kuna maeneo mengi ya kwenda kukusanya kodi na siyo maeneo haya. Mheshimiwa Waziri, ukipiria ripoti ya CAG imeonesha kuna kampuni kubwa zipo ambazo kimsingi zinaweza zikachangia ongezeko la kodi na mapato katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma Ripoti ya CAG imejieleza hapo. Imetueleza kuna kampuni za Kimataifa zinafanya kazi hapa na kampuni hizi kwa sasa ukiangalia uwezo wake ukisoma Ripoti ya CAG kuna kampuni zaidi ya 504 ambazo zipo na kampuni hizo ni zaidi ya 116 mpaka 154 hazijafanyiwa ukaguzi. Hebu twendeni tukajikite katika kuhakikisha ya kwamba kampuni hizi zinazoanzisha shughuli hizi za utoroshaji wa mapato twende tukatafute fedha kule tuwaache wachimbaji wadogo wadogo waweze kunufaika na rasilimali za nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe angalieni namna gani mnaenda kutupatia mitaji. Leo hii tunazungumzia habari ya mitaji kuna fedha zinatolewa asilimia 10, asilimia Nne zinaenda kwa vijana, asilimia Nne zinaenda kwa akina mama. Leo hii mchimbaji mdogo mdogo anayekopeshwa fedha hii anaenda kuchimba, bado hujajua kwamba ametumia gharama kiasi gani katika ku-invest, wewe unaenda kukaa katika soko kusubiri sasa umkate tozo ya ajira, umkate kodi mbalimbali bila kuangalia ametumia gharama kiasi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe hebu twende tukapitie upya mapendekezo haya. Mimi siyaungi mkono mapendekezo haya Mheshimiwa Waziri na nitashika shilingi. Nendeni, ukija hapa Mheshimiwa Waziri njoo na majibu ya namna gani unaenda kutusaidia wachimbaji waodgo wadogo na mkaondoe tozo hizi. Haya masharti ni magumu mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapozungumza Mheshimiwa Waziri mimi jimbo langu lina mgodi wa Bulyanhulu pale na Bulyanhulu kuna kampuni ambayo imeanzishwa Mheshimiwa Waziri iko pale. Wamezanzisha kampuni mbili kwa ajili, naweza kusema utoroshaji wa fedha. Kuna kampuni moja imeanzishwa ya TSL ambayo iko nje huko. Lengo la kampuni hii ni kupata purchasing activities ambazo zinaendelea. Lakini pia kuna kampuni nyingine TSL imeanzishwa Dar es Salaam hapa, leo hii mama ambaye analima nyanya Bulyanhulu hawezi akauza nyanya zake pale mgodini inatakiwa aende Dar es Salaam kwenye kampuni hiyo iliyoko kule na nyanya anapouza wale kazi yao ni ku- maximize profit tu kuongeza bei na kuhakikisha kwamba wanatorosha fedha katika maeneo yale. Nikuombe Mheshimiwa Waziri chonde chonde, sisi kama wachimbaji Mheshimiwa Waziri tuko tayari kulipa kodi lakini hatuko tayari kulipa kodi za namna hii. Nikuombe, sheria hii na mapendekezo haya yaende yakafutwe, yanaenda kuua Sekta ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani Mheshimiwa Waziri amenielewa katika Sekta ya Madini. Sasa niende katika kuzungumzia suala zima la biashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Tanzania ukiiangalia hapa tumezungukwa na nchi jirani. Mimi nilipata bahati ya kutembea kwenda Dubai nikaona namna gani wanafanya. Kuna maeneo mengi Mheshimiwa Waziri nikuombe, leo hii hapa unaona watu wa kutoka Uganda, Rwanda, kutoka maeneo mbalimbali wanaenda Dubai kwenda kununua magari wanayaleta yanapita hapa na yanaondoka. Hivi, kwanini kama Serikali Tusianzishe utaratibu wa kuwaruhusu watu hawa wanaoingiza magari wafungue yards kubwa hapa wasitozwe ushuru kwanza, watozwe tui le kodi ambayo kimsingi mteja akienda kununua gari lake ndiyo atozwe kodi. Maana yake ni kwamba tutawarahisishia watu wanaotoka Uganda, wanaotoka Burundi na maeneo mengine kuishia hapa nchini kwetu Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuambie watu wakazi wa Isaka tuko tayari kutoa eneo tuwaite hawa watu ondoeni kodi za magari watu walete hapa magari yao waweke. Mteja akienda pale anaponunua gari lake basi aweze kutozwa kodi na wale wanaotoka nchi jirani wanapokuja kununua magari hapa wasitozwe kodi wapeleke huko, hii itasaidia kuongeza mapato katika nchi yetu hii ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niende kwenye suala zima la kilimo. Tumeona mnajitahidi na nipongeze wakati tunajadili bajeti ya kilimo hapa watu wengi wamezungumzia walikuwa wanalia kilimo, kilimo, kilimo, lakini mimi nizungumze mambo mawili tu; katika kilimo hapa ni lazima tuone namna gani tunaenda kutengeneza masoko, issue sio mbegu, mbegu wananchi tunaweza tukanunua, lakini issue ni masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo ninapozungumza hapa kwenye Jimbo langu la Msalala wengi ni wakulima wa mpunga. Ukiangalia Kata ya Mwaruguru, Kata ya Jana, Kata ya Mwananse, Kata ya Kashishi, wote ni wakulima wa mpunga na tunavyozungumza hivi bado wana stock ya mwaka jana na bado wana stock ya mwaka huu na wameamua baadhi yao kutelekeza mpunga wao mashambani kwa sababu hawana sehemu ya kuupeleka na bei bado iko chini. Kwa hiyo, niwaombe namna gani Wizara inaweza kujikita katika kuhakikisha ya kwamba mnaenda kututafutia soko la kutusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Serikali imekuwa inakuja pale ambapo wananchi wanavuna ndio inaingia, lakini ni namna gani inamsaidia huyu kutafuta soko na kuhakikisha ya kwamba inamsaidia kwenye kumkopesha ili aweze kufanikiwa, hakuna. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri na niwaombe Wizara ya Kilimo hebu njooni sasa mfanye walau research katika Jimbo langu la Msalala ili muwasaidie wananchi hawa muone namna gani wanaweza wakauza mpunga wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu leo gunia la mpunga mwananchi anauza kwa shilingi 36,000 lakini bado kuna matapeli wameibuka humo humo. Leo Serikali imepiga marufuku lumbesa, lakini viwanda vimeibuka sasa kuanza kutengeneza mifuko ambayo inabeba madebe kuanzia nane, wanaenda kumdhulumu mkulima. Niwaombe Wizara na wanaohusika njooni basi katika Jimbo langu la Msalala muone namna gani wakulima hawa tunaweza kuwasaidia ili waweze kuuza mazao yao kwa bei iliyokuwa nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine niseme tu kuna matapeli wamo katika Wizara ya Kilimo na maeneo mengine. Ili tuweze kufanikiwa katika sekta ya kilimo; moja ni tunaweza kutafuta masoko nje ya nchi. Leo hii watu wanatoka nje kuja kufanya biashara ya mazao, kuna watu wanakuja kuwatapeli, ku-destroy image ya nchi; Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo uko hapo unanisikia, leo hii kuna watu wamekuja hapa kufanya biashara ya ufuta, Mheshimiwa Naibu Waziri ananisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watu hawa wamekuja kutuamini hawa wakatoa fedha zao hapa na wametapeliwa, chukueni hatua kwa watu hawa. Kesi hii Mheshimiwa Waziri bado inasumbuliwa, watu hawa wamedhulumiwa zaidi ya dola laki nne watu wamedhulumiwa na wafanyakazi hao wapo kwenye ma-go down wanawaleta watu kutoka nje, wanawaleta kuwaonesha kwenye ma-go down ya ufuta yale na wanawaambia ufuta huu sisi ndio tunaweza kuuza, wanapewa advance, kufanya hivyo ni ku-destroy image ya nchi na masoko katika nchi yetu hii Mheshimiwa Waziri. Mheshimiwa Naibu Waziri wa Kilimo uko hapo, hebu ninaomba hili suala lichukulie hatua, limeenda TAKUKURU, limeenda wapi, lakini hakuna majibu watu wanalia kutafuta fedha zao. Huyo aliyechukua fedha hizo Mheshimiwa Waziri mchukulieni hatua arudishe fedha, anaharibu taswira ya nchi Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo ninaomba kuunga mkono hoja na ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu, mama yetu kipenzi, mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Kwa ridhaa yako naomba basi nitumie style ya Mayele kumshangilia Mama Samia Suluhu Hassan kwani anaupiga mwingi sana. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, ninavyochangia hapa nina furaha sana baada ya kumwona Mwenyekiti wa Yanga Bunge, Mheshimiwa Gulamali baada ya kunikabidhi kadi yangu sasa ya Yanga kwanza. Sasa najijua ni mwanachama halisi wa Yanga. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie katika maeneo matatu na moja nianze na suala zima la nishati. Nianze kuipongeza Wizara ya Nishati kwa kazi kubwa ambayo inaendelea kuifanya, chini ya Waziri wake Mheshimiwa January Makamba na msaidizi wake Mheshimiwa Byabato. (Makofi)

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nimempongeza mwanachama wa Yanga kwa kuonyesha kadi yake na sio kadi tu, ni kadi ya viwango ya timu ya wananchi. (Makofi/Vigelegele/Vicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Kassim Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ninapokea taarifa hiyo na ninaomba nimshangilie na yeye kwa style ya Mayele. (Makofi/Kicheko)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, tunajua kwamba Yanga wanajitahidi kuigaiga ila tunawaomba waje na kadi za viwango. Simba ya Kimataifa tuna mpaka VISA Card, tuna kadi ya wanachama ya kiwango, ukiangalia kadi yao, yaani hadi wanatia huruma. Kwa hiyo, naomba mchangiaje aje achukue hizi kadi za Simba ili wakaboreshe za kwao zaidi kupitia Mwenyekiti wake wa Tawi. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo siipokei kwani Mheshimiwa Nicholaus Ngasa, Mbunge wa Igunga, ameniambia kuwa na kadi ya Yanga pia nimeanza kukopesheka kuwa na sifa. (Makofi/Kicheko)

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

T A A R I F A

MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, naomba tu kumpa taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Iddi kwamba, wananchi wanamsikiliza na hayo sio waliyomtuma, kwa hiyo aongee masuala ya wananchi. Ahsante sana. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, taarifa hiyo siipokei kwani waliyonituma hapa ni wananchi na nazungumzia wananchi. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, basi naomba niende moja kwa moja kwenye mchango wangu. Kwanza nianze kwa kuwapongeza Wizara ya Nishati kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya na hapa niwe mkweli kwamba, suala zima linaloendelea kwa sasa na hasa kwenye mitandao ya kijamii na baadhi ya wachangiaji jana juu ya upandaji wa bei za mafuta katika nchi yetu hii ya Tanzania. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niiombe Serikali kwamba katika mfumo huu ambao umeanzishwa na upo, mimi kama Mbunge wa Jimbo la Msalala, naendelea kuwaomba waendelee kuuboresha mfumo huu wa uagizaji wa mafuta. Kwani ni mfumo ambao ni bora sana na hata nchi zingine za jirani wanakuja kuiga mfumo huu hapa Tanzania. Ukiangalia Nchi za Malawi, Zambia tayari wamekuja kujifunza namna bora ya Serikali ya Tanzania tunavyofanya katika uingizaji wa mafuta ya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna hoja ambazo zimeibuka kwamba soko la mafuta liwekwe huria na wapewe wawekezaji binafsi waweze kuingiza mafuta. Nataka tu niuambie umma wa Watanzania kwamba, suala zima la uingizaji mafuta kwa pamoja lina faida zake katika nchi yetu hii ya Tanzania. Moja ya faida ya uingizaji wa mafuta kwa pamoja ni national security. Leo hii tunaangalia Nchi za Rusia na Ukraine vita inayoendelea kule, leo kama nchi tukiiachia soko huria la mafuta, upi sasa uhai na usalama wa nchi yetu hii? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba watu tunaochangia katika suala zima hili la mafuta tuweke uzalendo mbele, kuhakikisha , kwamba tunachangia ili kuleta manufaa ya nchi yetu. Nimeona wengi katika suala hili la mafuta wanachangia kuangalia masilahi yao binafsi. Niseme tu kuanzia leo utaratibu huu uendelee kwa sababu, ni utaratibu ambao unalinda uhai na usalama wa nchi yetu. Pia, leo kama mafuta yataachiwa liwe soko huria, sisi kama wafanyabiashara… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Kassim Iddi ngoja kwanza ni kazi yangu kuwalinda Wabunge humu ndani. Wale wenye mawazo tofauti na ya kwako umewasema hapo kwa ujumla kwamba wanachangia kwa masilahi yao binafsi; na Kanuni zetu zinasema mtu akiwa na masilahi lazima ataje na maslahi yake ya kifedha.

Sasa nataka kukurahisishia una njia mbili; moja, ni ya kusisitiza kwamba wana maslahi, kwa hiyo, sisi tutawataka wao walete hayo maslahi ambayo na wewe unayajua. Au ni kuondoa hiyo kauli ili kila Mbunge humu ndani awe huru kutoa mawazo yake, lakini kama unao uhakika huo, basi utalisema kwa namna hiyo. (Makofi)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, naomba kuondoa kauli hiyo, lakini niendelee kusisitiza kwamba, tunapokwenda kuchangia ni lazima tuangalie maslahi ya wananchi wetu ambao wametutuma.

Mheshimiwa Spika, niendelee kwa kusema kwamba upatikanaji wa mafuta kwa bei ambayo iliyopo sasa ni utaratibu ambao ni wa Serikali umeendelea kudhibiti mfumuko wa bei kupanda na kushuka na kuhakikisha kwamba, hao waagizaji wa mafuta wanaagiza kwa pamoja, sambamba na kutangazwa tender ya pamoja ili kuweza ku- control bei ya soko la Kimataifa. Kwani tunafahamu kwamba hata visima vya mafuta vinavyouza mafuta haviuzi moja kwa moja kwa muuzaji wa mafuta ama kampuni yoyote, isipokuwa wameteua ma-agent kwenye nchi zao huko ambao wanauza mafuta kwenye nchi nyingine hizi za jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kusisitiza kwamba utaratibu huu Serikali iendelee kuuboresha vizuri, lakini niishauri tu kwamba hapa suala ni kuhakikisha ya kwamba wanajitahidi sasa, kuangalia zile gharama na kodi mbalimbali ambazo zimewekwa waweze kuzifanyia kazi, waziondoe ili kupunguza gharama ya mafuta. Tukumbuke sakata hili linafanana moja kwa moja na sakata la vinasaba. Wapo waliokuja hapa wakasema Kampuni ya GFI haifai inatunyonya na Serikali ilisikia ushauri huo ikaenda kuondoa na kuwapa TBS. Hata hivyo, baada ya siku tu kupita wale wale waliokuwa wanaipiga vita GFI walirudi wakaanza kusema kwamba sasa TBS haina uwezo, baada ya kuona sasa mianya ya mafuta yameanza kuingia ambayo yanachakachuliwa. Kwa hiyo, niombe tunapokwenda kujadili hili suala hasa katika kuzingatia usalama wa nchi yetu tuweke uzalendo mbele.

Mheshimiwa Spika, niendelee kuchangia sasa upande wa TAMISEMI. Hali ya barabara katika maeneo yetu ni mbaya sana na hasa nizungumzie sasa kwenye Jimbo langu la Msalala. Barabara ni mbovu sana. Leo hii tunazungumzia ukuaji wa kilimo kwenye maeneo yetu, leo hii tunazungumzia ukuaji wa viwanda kwenye maeneo yetu, lakini vyote hivi haviwezi vikaenda sambamba kama miundombinu ya barabara haitarekebishwa. Niombe Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, Mheshimiwa Naibu Waziri nadhani yupo hapo ananisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto kubwa sana kwenye maeneo yetu haya, hasa katika usimamizi wa fedha ambazo zinakwenda kwenye kukarabati barabara. Leo hii utaona tender nyingi za barabara zinatangazwa wakati wa mvua. Niendelee kuwaomba Mheshimiwa Waziri na Wizara kwa pamoja waweke mkakati sasa wa fedha hizi ambazo tutakuwa tumezipitisha kwenye bajeti, ziende zikaendelee kukaa pale hata wakati wa mvua zisiende zikachukuliwa tena huko mbele. Pia, waweke usimamizi madhubuti katika kuhakikisha kwamba wakandarasi wanaopatikana kwenye maeneo yale ni wakandarasi ambao moja, wana sifa za kuhakikisha ya kwamba wanatekeleza miradi ile kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, wakandarasi hao wawe financially fit kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miradi ile wanakwenda kuitekeleza bila kusuasua na wala kutegemea mikopo kwenye mabenki. Kwani kuwapa wakandarasi ambao hawana uwezo kwenye maeneo yetu ndio kunapelekea kucheleweshwa kwa barabara nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, leo hii nitazungumzia miradi katika eneo langu la Kata ya Jana, Kata ya Mwaruguru, Kata ya Mwanase, maeneo haya ni wakulima wa mpunga. Nimpongeze Mheshimiwa Bashe kwa kazi kubwa aliyoifanya ya kugawa vitendea kazi kama pikipiki na kuendelea kuthibitisha kwamba mama yetu Samia Suluhu ametoa fedha nyingi kwenye kilimo. Matunda hayo hayawezi yakaenda kuleta matokeo kama barabara zetu kwenye maeneo ya uzalishaji zitakuwa ni mbovu. Leo hii tunaongea barabara hizo hazipitiki. Niiombe Wizara wajaribu kuangalia namna gani na njia bora ya kuhakikisha kwamba barabara hizi zinaanza kutengenezwa mapema kabla ya mvua, ili wananchi sasa wa kwenye maeneo yale waendelee na uzalishaji katika maeneo hayo. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2022
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika nchi yetu hii. Tunaona kabisa katika sekta ya nishati, umeme vijijini kuimarisha miundombinu ya umeme, ujenzi wa uzalishaji umeme katika maeneo mbali mbali, kazi inaendelea. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Nishati, Mheshimiwa January Makamba, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu lakini pia Mkurugenzi Mkuu wa REA vijijini kwa kazi kubwa ambayo wananendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri mara nyingi akisimama hapa anazungumzia habari ya nishati kwamba ni mambo matatu. Jambo la kwanza anasisitiza habari ya uzalishaji na sina shida na uzalishaji, naomba nimpongeze sana kazi nzuri inaendelea kwenye uzalishaji. Jambo la pili anazungumzia habari ya usafirishaji, sina shida na usafirishaji kwa sababu miundombinu mpaka sasa inaendelea kurekebishwa na naamini baada ya muda mchache miundombinu hii itakuwa tayari imekaa vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la tatu ni suala la usambazaji wa umeme na hapa nilitaka nijikite kwenye kuzungumzia kwenye suala nzima la usambazaji. Nijikite kwenye Wilaya yetu ya Kahama. Wilaya ya Kahama ina halmashauri tatu ina vijiji zaidi ya 323, na tuna mkandarasi mmoja tu anayesambaza umeme wa REA ambaye bado mpaka sasa ana mkataba wake unaosema ni ndani ya miezi 18 awe amemaliza. Hata hivyo, mpaka sasa ni asilimia 23 tu ya kazi aliyoweza kuifanya kwenye Wilaya ya Kahama.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, Mkandarasi huyu anayesambaza uememe kwenye Wilaya ya Kahama kwa maana ya Majimbo matatu; Ushetu, Msalala na Kahama, bado uwezo wake unaonekana kuwa chini sana kwa sababu mpaka sasa ameshamaliza miezi saba na miradi bado ipo asilimia 23 tu. Nikuombe Mheshimiwa Waziri na hapa niombe uchukulie Wilaya ya Kahama kama special case, kwa sababu Wilaya ya Kahama ni Wilaya kubwa ina vijiji vingi ina halmashauri nyingi. Tumeahidi wananchi wetu kwamba ndani ya miezi 18 umeme huu utakuwa umekamilika kusambaa kwenye vijiji vyote.

Mheshimiwa Naibu Spika, mathalani kwenye Jimbo langu la Msalala tuna zaidi ya vijiji 62 havijapatiwa umeme. Sambamba na hili tuna migodi mikubwa na midogo ambayo inaenda na inakuwa kwa kasi na inategemea nishati. Mheshimiwa Waziri wewe mwenyewe utakuwa shahidi ulifanya ziara kwenye Jimbo la Msalala na ulienda kwenye maeneo ya migodi, ulitembelea Ntambalale, ulitembelea Mwanzimba na maeneo mengine na uliahidi kwamba umeme baada ya wewe kutoka umeme utaenda; lakini mpaka leo Mheshimiwa Waziri bado umeme haujafika kwenye maeneo hayo. Ninaomba muichukulie Wilaya hii ya Kahama kama special case ni tofauti na Wilaya nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, wilaya nyingine utaona kijiografia eneo lao ni dogo sana tofauti na Wilaya ya Kahama. Ukichukua Jimbo la Msalala tu lenye kata 18 lina square mita nyingi sana, kazi iliyofanyika ni kata moja na maeneo machache sana mapka sasa. Kwa hiyo niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini cha kushangaza hapa wamemuongezea tena mkandarasi huyu zile kilometa zingine mbili kwenye kila kijiji. Kazi ya kwanza bado hajamaliza na yuko asilimia 23 lakini mmeenda tena Mheshimiwa Waziri kumuuongeza tena extension ya umeme kwa kilometa mbili kila kijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa wasiwasi wangu ni kwamba wananchi tumewaahidi ndani ya miezi 18 umeme utakuwa umekamilika na wamepatiwa huduma hiyo; na baadhi ya wananchi tayari wameshafanya wiring kwenye nyumba zao. Sasa kama tu kazi ya kwanza ambayo zaidi ya vijiji 323 hajamaliza, je, tumemuongeza tena kila kijiji hicho hicho kilometa mbili, kwa maana ya nguzo 40. Je, kazi hii itakamilika kwa wakati?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri baada ya hapa, mimi naomba tukae, tuwasiliane tuzungumze tuone namna ya kukaa mkandarasi huyo ili atahakikishie, kama uwezo ni fedha ama kuna mambo memngine basi muone Wizara mnaweza kumsaidiaje.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie usambazaji wa umeme kupitia TANESCO. Tunafahamu kwamba TANESCO kwa sasa bado wana fedha, Wilaya ya Kahama tuna bajeti ya fedha ya kuweza kusambaza umeme kwenye maeneo mengine. Changamoto ya sasa ni nguzo. Sasa Mheshimiwa Waziri naomba utusaidie kwamba kama fedha tunayo Wilaya ya Kahama lakini nguzo hazipatikani naomba Wizara itusaidie ili nguzo hizi ziweze kupatikana na wananchi waweze kupata huduma ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia naomba nijielekeze kwenye sekta ya madini, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Madini kwa kazi kubwa ambayo anayoendelea kuifanya. Leo hii utaona mchimbaji na Mtanzania wa kawaida anamiliki leseni.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sasa niseme tu, pamoja na kazi kubwa anayoendelea kuifanya kumekuwa na baadhi ya watu wanamvuta shati nyuma. Sisi kama Kamati tunaendelea kukupa moyo tunasema kwamba wale ambao wanakuvuta shati nyuma. Tutaenda kupamba nao ili kufanikisha adhma ya kuhakikisha unachangia asilimia 10 kwenye Pato la Taifa. Mambo ambayo yanamkwamisha Mheshimiwa Waziri, na hili nimuombe sana Waziri wa Fedha; Wizara ya Fedha imekuwa ni kikwazo kikubwa sana kwenye sekta ya madini. Leo tunazungumzia habari ya umiliki wa leseni; na niwapongeze sana Mtendaji Mkuu wa Tume na Mheshimiwa Waziri, wameweza kuwapatia leseni wengi, wananchi wanajivunia kuwa na leseni. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama alivyosema dada yangu hapo Mbunge wa Viti Maalum hapo, Nusrati Hanje, kwamba sasa mahitaji makubwa kwa wachimbaji ni mambo mawili tu. Jambo la kwanza ni hitaji la mtaji; na hapa niombe sana BOT, ambao mara kwa mara wamekuwa wakisisitiza benki kuwakopesha wachimbaji wadogo wadogo lakini benki hizo zimekuwa in reality haziendi kuwakopesha wachimbaji wadogo wadogo. Wachimbaji wadogo wadogo wanalia, leo hii wana leseni lakini wamekosa mitaji. Kwa hiyo, niendelee kuomba sana Wizara ya Fedha na hasa BOT kwenda kuhakiki kwamba ni wachimbaji wangapi ambao wameshakopeshwa fedha na benki hizi ambazo mpaka leo zinaweza kuwasaidia katika uchimbaji wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini la pili ni suala linalohusu ripoti ya GST. Nipongeze sana kazi kubwa ambayo inafanywa na GST; na nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, ikimpendeza hebu tuone namna ya kutenga fedha ya kuiwezesha GST ije iweke maabara ya upimaji wa madini katika Wilaya ya Kahama ili wananchi wanaozunguka Wilaya ya Kahama, ambako ndiko madini mengi yanatoka waweze kupata fursa ya kupimiwa madini yao kwa uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini si hivyo tu, niendelee kuomba sana muweze kutenga bajeti kubwa kuiwezesha GST iweze kununua mitambo ya drilling ili iweze kufanya tafiti za kutosha. Mchimbaji mdogo mdogo huyu anayemiliki leseni akiweza kupatiwa mtaji, akaweza kupatiwa data za kwenye eneo lake maana yake ni kwamba tutakuwa tumemkuza mchimbaji mdogo mdogo huyu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri anapambana na mambo mengi sana kwenye Wizara hii; lakini pia aende sasa matapeli yaliyoko kwenye Wizara hii. Leo utaona Mheshimiwa Waziri watu wanatoka huko nje na briefcase wanakuja hapa. Watanzania tunaomiliki leseni na rasilimali tunabaki kuwa maskini lakini hizi kapuni nyingine; na hasa niseme tu, zile zinazotoka nje, zinakuja na briefcase pekee, lakini hapa wakiondoka wanaondoka na fedha nyingi zimejaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba kuna kampuni moja, na Mheshimiwa Waziri nikuombe sana, kampuni hii wewe mwenyewe unaifahamu, ni QATAR Mining. Hii inachukua fedha kwenye benki zetu hizi hizi, lakini pia inachukua fedha za Watanzania. Vilevile imeanza kudhulumu hawa watu. Niombe uchukue hatua za haraka sana kwenye kampuni hii ambayo inaendelea kudhulumu Watanzania, Watanzania waweze kupata haki zao za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii kwa niaba ya Wananchi wa Jimbo la Msalala ili nichangie hotuba ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kwa moja nianze kwa kuipongeza Wizara ya Maji kwa kazi kubwa inayoendelea kuifanya. Pia niishukuru Serikali kwa kuona umuhimu wa sasa wa wananchi wa Jimbo la Msalala kupata maji safi na salama. Pia tutakuwa wachoyo wadhila kuishukuru Serikali kwa fedha nyingi ambazo wametutengea sisi Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetutengea kiasi cha Sh.4,600,000,000.00 kwa ajili ya miradi mbalimbali katika Jimbo langu la Msalala. Kwa kweli kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala tunakushukuru sana Mheshimiwa Waziri, tunaishukuru sana Serikali lakini pia tunamshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeweza kutengea kiasi cha shilingi milioni 558 katika mradi wa maji ambao utahudumia Vijiji vya Nduku, Ntobo, Busangi. Niombe baada ya fedha hizi kutoka basi ziende haraka iwezekanavyo ili kukamilisha mradi huu ambao ni changu na utaweza kupunguza tatizo la maji katika Kata hii ya Busangi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri na Serikali haijaishia hapo tu, wameenda kutupatia kiasi cha shilingi milioni 250 kwa ajili ya extension katika mradi mkubwa wa maji. Hata hivyo, kuna mradi mkubwa ambao unaitwa Manguirogi ambao ni joint venture kati ya Serikali na Mgodi, hii ni fedha ya CSR. Namwomba Mheshimiwa Waziri baada ya Bunge hili akubali kuambatana nami ili twende kule tukaangalie ili tuweze kufahamu ni kiasi gani Serikali imeweza kuchangia katika mradi huu lakini pia mgodi umechangia kiasi gani? Fedha hizi ni za CSR na tunatamani sana tuone ili tujue chenji yetu imebaki kiasi gani ili kusaidia kusambaza maji katika Kata za Runguya, Ipinda, Segese na maeneo mengine. Mradi huu unatoka Mangu unaishia Irogi, niiombe Serikali bsi iweze kutenga fedha tena kwa ajili ya kufanya extension katika maeneo ya Ikinda Kata za Lunguya, Nyangarata, lakini na maeneo mengine ili kuweza kusaidia na kupunguza tatizo la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Kata ya Segese inakua kwa kasi sana kwa sasa na matarijio yetu ni kuhakikisha kwamba tunapata maji ya ziwa ili watu waweze kunufaika. Pia tuna Makao Makuu ya Ntobo ambayo kimsingi tunaenda kuyazindua muda si mrefu, niombe mradi huu unaotoka Nduku kuja Ntobo lakini pia mradi huu unaotoka Mangu kuja Irogi extension iweze kufanyika pia maji haya yaweze kusogea katika Makao Makuu ili ituwezeshe kuwafikishia wananchi miundombinu hii ya maji na tuweze kuwahimiza sasa waweze kuwekeza kwa kiwango cha juu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna mradi mkubwa ambao umeshakamilika wa Kagongwa – Isaka. Mheshimiwa Waziri kama anakumbuka alikuja kuzindua na Mheshimiwa Rais alikuja pale na alitaja mbele ya Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kwamba kuna chenji imebaki. Pia mradi huu unapita katika Kata ya Mwakata ambayo haina maji. Naomba Waziri aone ni namna gani chenji iliyobaki katika mradi unaotoka Kagongwa kwenda Isaka mnaweza kuzipeleka katika Kata ya Mwakata ili sasa na wakazi wa Kata ile waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali na Mheshimiwa Waziri kwa kututengea kiasi cha shilingi 1,500,000,000 katika Kata za Jana na Mwalugulu. Ni matumaini yangu kama fedha hizi zitaenda haraka na kufanya uzinduzi wa mradi huu utasaidia sana wakazi wa Kata hizi ili na wao waweze kunufaika na mradi huu wa maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kusema kwamba kumekuwa na changamoto ya bili za maji, nimwombe Mheshimiwa Waziri wakati anakuja kutembelea mradi huu Mangu - Irogi tupate fursa ya kutembelea wananchi na kusikiliza kilio chao juu ya ongezeko la bili za maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Wizara ione namna gani wanaweza wakaja na solution ya kuhakikisha kwamba wanatengeneza mfumo mpya ambao utasaidia kupunguza adha ya ongezeko la bili la maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, siyo hivyo tu, niiombe Wizara iweze kuwapatia mafunzo maalum wale wasimamizi kule chini. Hii itawasaidia kutumia miradi hii ya maji ambayo inapelekwa kule na inatumia gharama kubwa ili waone namna gani sasa wanaweza kuanza kusambaza katika miji ya watu na ili wakazi wa maeneo yale waweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishie hapo, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kunipatia nafasi hii kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala. Nami naomba nichangie hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa niende moja kwa moja kwa kuipongeza Wizara kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya katika Taifa letu hili la Tanzania. Pia, niende moja kwa moja kuipongeza Serikali kwa kufikiria na kuanza ujenzi wa standard gauge kwa maana ya kwamba reli ya kati na kufikiria kujenga bandari kavu katika Kata ya Isaka ambayo matumaini yetu kama wana Msalala ni kuhakikisha ya kwamba bandari hii itakapokamilika itaenda kukuza uchumi wa Jimbo la Msalala katika kata ya Isaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja kwa kuipongeza Wizara na hasa bandari kwa kutupatia mabati 300ya CSR kwa ajili ya ukamilishaji wa kituo cha afya katika Kata ya Isaka. Ahsanteni sana, kwa niaba ya wana Msalala tunawashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende moja kwa moja nizungumzie suala la barabara katika Jimbo langu la Msalala. Hali za barabara katika Jimbo langu la Msalala ni mbaya sana. Nimekuwa nikipiga kelele hapa suala la barabara inayotoka Bulyanhulu – Kahama. Barabara hii ni muhimu sana katika uchumi wa Tanzania kwani wote ni mashahidi ya kwamba Serikali yetu inapokea fedha nyingi sana kutoka katika Mgodi ule wa Bulyanhulu lakini barabara hii inahudumia wakazi wengi sana wa Jimbo la Msalala lakini pia wa Mkoa wa jirani wa Geita. Lakini, ndiyo shortcut
ambayo mtu anaenda Geita, ni rahisi kwake kupita pale katika Jimbo la Msalala kuelekea maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii kama nilivyosema hapo mwanzoni kwamba kuna fedha imetengwa na nikaomba Wizara ya Ujenzi, Madini na nikamuomba Waziri wa fedha wakae kwa pamoja waone namna gani fedha hizi zinaweza zikatoka kwenda kukamilisha barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimeona hapa kama Wabunge wenzangu walivyochangia kwamba ni ukweli usiopingika kwamba tunaona kabisa kama Mbunge mwenzangu Kunambi amesema kwamba anashangaa ni vigezo gani vinatumika Wizarani katika kugawa fedha hizi. Nimeona hapa barabara hii Geita – Bukoli – Kahama imetengwa kwenye route tatu na route tatu hizi ukiangalia Geita kwa maana ya kwamba Bulyanhulu junction road wametenga kiasi cha shilingi bilioni 1.5 lakini hivyo hivyo junction road to kahama wametenga bilioni 1.5.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ukiangalia hapa barabara nyingine ambayo inaenda Uyoga – Nyamilangano, barabara ile ile route ile ile, wametenga kiasi cha shilingi bilioni 3, usawa uko wapi? Mmetenga kiasi cha shilingi bilioni 6 kwa maana ya kwamba mmetenga route tatu. Kwanini route ya kwanza mmempa bilioni 1.5, route ya pili mmetupa bilioni 1.5, halafu route ya tatu mkampa bilioni 3? Basi toeni hiyo bilioni 1 mtugawanyishe huku milioni 500, 500 ili wote twende sawa bilioni 2, 2 Mheshimiwa Waziri, nadhani unanisikia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba Mheshimiwa Waziri, barabara hii japo ina urefu wa kilometa 160 lakini kilometa zilizotengwa hapa ukiangalia ni jumla ya kiasi cha shilingi bilioni 6 ambayo ni kilometa 6 tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niendelee kuwapongeza na kuwaomba barabara muhimu naona hapa tumetengewa barabara ambayo inatoka Ntobo – Busangi – Ngaya – Buluma – Jana mpaka Didia mmeitengea kiasi cha shilingi milioni 170 kwa kutengenezwa kiasi cha kilometa 4.8 lakini mmeenda tena mnatutengea kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya kilometa 2.8.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ina urefu wa kilometa 85 lakini ukiangalia hapa ni kilometa kama saba ndiyo mmetutengea hapa. Barabara hii ni muhimu katikauchumi wetu huu wa Jimbo la Msalala. Barabara hii inahudumia Kata ya Ngaya, Kata ya Jana, Kata ya Kashishi na maeneo yote haya ni wazuri wa kuzalisha mpunga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kilimo cha mpunga, unapozungumzia mpunga asilimia 85 ya mpunga unaopatikana Kahama unatoka katika Jimbo la Msalala kwenye kata hizi. Matumaini yangu ni kwamba barabara hii ikienda kuimarika itainua uchumi wa Jimbo langu la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri, barabara hii muendelee muichukue moja kwa moja. Muimiliki, namaanisha kwamba muiingize kwenye matengenezo ya kila mwaka ili wananchi…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana. Kengele imegonga Mheshimiwa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, ninaomba niunge mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru kwa kunipa fursa hii ya kuchangia kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala, ninaomba nichangie kwenye hotuba hii ya bajeti ya Wizara ya Mawasiliabo. Kwanza kabisa, naomba nijielekeze kwenye suala zima la usalama wa fedha za mtu anaye-transfer fedha kutoka kwenye mtandao mmoja kwenda kwenye mtandao wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na changamoto kubwa kwa watumiaji wa mitandao wanaofanya transfer kutoka mtandao mmoja kwenda mtandao wa pili juu ya usalama wao wa fedha mahali ambapo wanakosema kutuma fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano na mwenyewe ni muathirika, mimi ni mtumiaji wa mtandao wa Airtel na inapotokea bahati mbaya ninatuma fedha kwenda kwenye mtandao mathalani wa Vodacom, inapotokea nimekosea usalama wa fedha unakuwa ni mdogo. Kwa hiyo, naomba nishauri Wizara iweze kuona namna gani basi sasa ianze kushauri kampuni hizi zijikite katika kuhakikisha kwamba wanaweka coordination ili ku-secure zile fedha za mtumiaji anayetuma mtandao mmoja kwenda mtandao wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze moja kwa moja kwenye Jimbo langu sasa la Msalala. Jimbo langu la Msalala lina kata 18 na lina vijiji 92 lakini katika Kata zaidi ya 12 hatuna mawasiliano. Kumekuwa na changamoto nyingi sana juu ya ukosefu wa mawasiliano katika Jimbo langu la Msalala na hasa katika Kata ya Jana, Mwaruguru, Mwanase, Kashishi, Lunguya, Ntobo, Shilela, Mega na kata nyingine nyingi. Matatizo haya yanasababisha sasa ndoa kuvunjika. Leo hii katika maeneo mbalimbali katika Jimbo langu la Msalala ukitaka kupiga simu mpaka utafuta mti au mbuyu mrefu ili uende ukapige simu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo haya nimeshawasilisha kwa Waziri na nimemuomba Waziri kwamba aone namna gani anaweza kutusaidia sisi wa Jimbo la Msalala ili tuondokane na adha hii. Ndoa nyingi zinavunjika kwa sababu ya kisingizio cha mtu kwenda kwenye mlima fulani kupiga simu, unakuta ameshaandaa mchepuko hukohuko. (Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukosekanaji wa mawasiliano haya unahatarisha sasa ndoa za wananchi wangu wa Jimbo la Msalala. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, chondechonde, makao makuu ya wilaya hatuna mtandao. Wanapotaka kuchapisha document za halmashauri ni mpaka wasafiri waende Kahama Mjini, Mheshimiwa Waziri hebu tuangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hilo tu, tuna maeneo mengi ya machimbo katika Jimbo langu la Msalala. Kama mnavyofahamu suala zima la biashara ya madini na biashara nyingine linaenda kimtandao, lakini suala la applications mbalimbali linaenda kimtandao, ukosekanaji wa mawasiliano katika Jimbo langu la Msalala, hasa katika Kata ya Segese, Kata ya Bulyanhulu, Kijiji cha Nyangalata, Kata ya Jana na maeneo mengine, unasababisha kuwanyima haki wananchi juu ya kufanya application ya kuomba leseni za madini na kibali cha mazao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama mnavyofahamu wananchi wetu ili kupata kibali cha kusafirisha mazao unatakiwa u-apply kwa mtandao na maeneo yale hayana mtandao. Mheshimiwa Waziri ukosefu wa mawasiliano katika Jimbo la Msalala unasababisha anguko kubwa la kiuchumi. Tunakuomba chondechonde katika kata hizi ambazo nimezitaja angalia namna gani basi unaweza kutupatia mawasiliano, ili wananchi wetu waweze kuondokana na adha hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yangu yalikuwa ni hayo. Naunga mkono hoja, naomba Mheshimiwa Waziri chondechonde akina mama na akina baba wanalalamika ndoa zao ziko hatihati, tuangalie kwa jicho la huruma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru kwa kunipatia nafasi hii na mimi niweze kuchangia hotuba ya bajeti ya Wizara ya Ulinzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Amiri Jeshi Mkuu Rais wetu wa Jamhuri ya Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya na niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwa heshima na taadhima kabisa kwa kutoa heshima kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tugonge meza mara mbili ili tuonyeshe heshma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ninaomba nimpongeze Jenerali Mabeyo kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya ya kudumisha amani katika nchi yetu hii ya Tanzania. Lakini pia niipongeze Wizara na Waziri Mheshimwia Elias Kwandikwa, jirani yangu, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika Wizara hii ya Ulinzi lakini mwisho kabisa niwapongeze majenerali na mabregedia wote walioko hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba sasa na mimi nianze kuchangia katika hotuba ya bajeti hii. Moja kabisa tunafahamu ya kwamba JKT kwa sasa wameingia katika ushindani wa kuwekeza lakini wameenda mbali Zaidi katika kuhakikisha ya kwamba wana-compete zabuni mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kuchangia kwa maana ya kuiomba Wizara hasa JKT kumekuwa na ucheleweshaji wa miradi inayotekelezwa na jeshi letu la JKT. Nimuombe Waziri Mheshimiwa Waziri utakuwa ni shahidi katika Jimbo langu la Msalala tunao mradi mkubwa wa ujenzi wa jengo la Utawala katika Halmashauri ya Msalala ambayo inatekelezwa na JKT na Mheshimiwa Waziri niseme tu kwamba ukiangalia fedha iliyotengwa walitoa certificate ya kiasi cha shilingi milioni 515 kwa ajili ya hatua za awali za ujenzi wa jengo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini sambamba na hilo ucheleweshaji umeendelea kuimarika jengo hilo mpaka tunapozungumza sasa bado halijakamilika japo kuna jitihada ambazo zinaendelea. Niombe Wizara Mheshimiwa Waziri unanisikia upo hapo ndugu yangu, jirani yangu, tunapata tabu sana wananchi wa jimbo la Msalala Halmashauri yetu tumekaa katika sehemu ya kupanga tumebanana tunahitaji sasa tuhamie kwenye jengo hilo, niiombe Wizara, niwaombe JKT kumaliza mradi huu kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na malalamiko juu ya wastaafu wetu, juu ya namna gani kuiomba Wizara na Serikali waweze kuwaongezea pension. Kama unavyofahamu wastaafu hawa baada ya kustaafu wanarudi vijijini kuja kujumuika na wananchi, kumekuwa na changamoto nyingi juu ya changamoto za kimaisha katika wastaafu hawa. Niiombe Wizara iweze kuona ninamna gani basi wanaweza kuongeza walau pension kidogo ili wasaidie wastaafu wetu hawa kuendesha maisha yao huko walipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia kwa kuwa Jeshi linatoa mafunzo mbalimbali, nikuombe kabla wastaafu wetu hawa hawajastaafu basi ni vyema Wizara ikae na kupanga waone namna gani basi wanaweza wakaanzisha short course ya kuwaandaa wastaafu wetu hawa wanapostaafu waende wakakabiliane na maisha ya huko vijijini. (Makofi)

Kwa hiyo, ni ukweli usiopingika kwamba wazee hawa, wastaafu hawa wanapokuja kule ni kweli usiopingika kwamba wanazalilika sana maisha ni magumu mno, wanapokuja kuanza ku-adopt mazingira ya kule vijijini wanapata taabu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona kwamba kumekuwa na malalamiko kwamba Mbunge mwenzangu amechangia hapa juu ya namna gani askari wetu wanajeshi wetu hawa wanapatiwa mavazi pair chache na ameshauri kwamba ikiwezekana walau waweze kupatiwa pair tatu. Lakini ni ukweli usiopingika kwamba Jeshi lina taratibu zake na taratibu za namna gani kuweza kutoa mavazi haya unaona kabisa hapa wanatakiwa wapewe mavazi mapya ya ndani ya miezi sita. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa ninavyozungumza bado baadhi ya wanajeshi hawa hawajapatiwa mavazi hayo mapya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri, vijana wetu hawa wanafanya kazi kubwa sana, lakini pia na wao wanahitaji wapate mavazi haya ili waonekane smart kama watu wengine, niiombe Wizara kama kunauwezekano basi Wizara ione namna gani inaenda kuwapa mtaji Jeshi la JKT, ili wafungue kiwanda cha kushona mavazi hawa wanajeshi wetu. Kwa kufanya hivyo tutasaidia kutengeneza ajira, lakini tutakuwa tumewajengea vijana wetu ili tuweze kuondokana na adha ya upungufu wa mavazi na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho nimalizie kusema kwamba kumekuwa hakuna usawa juu ya usaili wa vijana wetu huko chini katika ngazi za chini katika kujiunga na Jeshi letu. Taarifa katika baadhi ya maeneo zinakuja leo kesho usaili umekwisha, kwa hiyo, niiombe Wizara ione namna gani inapotoa taarifa za usaili za vijana wetu hawa wapeleke mapema kule, lakini kumekuwa kuna urasimu pale mikoani, vijana wetu hawa baadhi wanaobahatika kuingia katika nafasi hizo wanapofika mkoani wanapewa vikwazo vingi vingi na wengine wanatolewa majina yanakuwa yameandaliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nikuombe Mheshimiwa Waziri, sisi wana Mkoa wa Shinyanga ni waathirika wa hilo, hebu tuangalie tuone namna gani sasa Wizara inaenda kujipanga kuonesha ya kwamba inaondoa urasimu huo ili vijana na wao wapate sifa ya kujiunga na Jeshi letu hili la wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kumalizia naomba niendele kuwapongeza na ninaunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia kwenye hotuba hii ya Utumishi. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Rais wetu mpendwa, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kutoa kibali cha promotion kwa wafanyakazi wote nchini kwa bajeti tatu mfululizo kwa maana ya 2018/2019, 2020/2021 na 2019/ 2020. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapozungumzia leo habari ya watumishi, sitapenda kuacha kutoa pongezi nyingi sana kwa Waziri Mkuu wetu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya na harakati zake za kuwa mstari wa mbele katika kuhakikisha ya kwamba anawasemea watumishi na kutetea maslahi ya watumishi nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya na kaka yangu Mheshimiwa Ndejembi, wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kuchangia mambo machache sana kwa siku ya leo. Wamezungumza hapa suala zima la mafao, sitataka kulirudia, lakini nataka nikazie tu kwamba, hata kwenye Jimbo langu la Msalala, suala zima la mafao kwa wastaafu limekuwa ni changamoto kubwa sana, hasa kwenye familia ambazo wamepoteza watu wao ambao wanastahili kupewa hayo mafao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatolea mfano leo kwenye Kata ya Burige kuna mama mmoja alifiwa na mume wake Mtendaji wa Kijiji, leo hii tunazungumza ni zaidi ya miaka kadhaa sasa, bado hajapatiwa mafao ya mume wake ili yaweze kumsaidia katika harakati za kusomesha watoto wake na kulea familia yake. Kwa hiyo, naendelea kuomba na kusisitiza Wizara waone namna gani wanaweza kuboresha mfumo huu wa mafao ili wastaafu waweze kupatiwa mafao yao kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatambua hapo zamani tulipokuwa na Mfuko wa LAPF na PSSF tunaona changamoto hizi zilikuwa ni chache sana, lakini sasa baada ya kuundwa mfumo huu changamoto zimekuwa ni kubwa sana. Kwa hiyo, naendelea kumwomba dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama kuhakikisha ya kwamba wanalitilia suala zima la mafao ya wastaafu waweze kupata kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kuzungumzia suala zima la upungufu wa watumishi. Katika Jimbo langu la Msalala tuna upungufu wa watumishi takribani 500. Kama alivyochangia Mheshimiwa Mbunge mwenzangu hapo, kwamba sisi tunaotoka katika Majimbo ya vijijini, hali ya mazingira katika maeneo yale ni ngumu sana. Watumishi hawa wanaishi katika mazingira magumu mno. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao upungufu mkubwa wa watumishi, wengi wao wanahama katika maeneo yale kutokana na mazingira magumu ya pale. Siungani na Mheshimiwa Tabasam kwa hoja aliyoisema hapa kwamba wanatakiwa wahame kwa sababu wanatakiwa waolewe. Nasema mazingira magumu na mikopo ndiyo inayowafanya watumishi katika maeneo yetu hasa katika kada ya Ualimu, Afya na maeneo mengine waondoke katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ije na mfumo, ikiwezekana waweze kutafuta hata taasisi moja, ambayo itaweza kuwatafutia mikopo isiyokuwa na riba. Watumishi hawa hasa walimu katika maeneo yetu wanakopa sana VICOBA kutokana na hali ngumu ya maisha iliyoko kule. Leo hii utaniambia kwamba mwalimu anakwenda kufundisha darasani, lakini kila wakati anapigiwa simu za madeni na riba kubwa ambazo yeye mwenyewe katika mshahara hawezi kupokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakuomba dada yangu Mheshimiwa Jenista Mhagama uangalie namna gani ya kutafuta, ikiwezekana uongee na Taasisi za kibenki, ambazo zitaweza kuweka mfumo mzuri kuwasaidia hawa watumishi wetu huko waweze kupata mikopo yenye riba nafuu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwamba upungufu wa watumishi katika Jimbo la Msalala ni mkubwa sana, na nizungumzie katika Idara ya TAKUKURU. Wilaya ya Kahama ina Halmashauri tatu, lakini nimefanya utafiti, Wilaya nzima, tunao watumishi 10 tu wa TAKUKURU. Katika watumishi 10 hao, ni wanne tu ambao wanafanya kazi za kwenda kufanya investigation huko katika Halmashauri hizi. (Makofi)

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Cherehani.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mchangiaji anachangia katika Wilaya ya Kahama na katika Jimbo la Ushetu pia Mheshimiwa Rais anapeleka fedha nyingi sana, lakini hatuna watumishi wa TAKUKURU wala Ofisi ya TAKUKURU; pia, anavyoongea mchangiaji nataka nimpe taarifa kuwa katika Jimbo la Ushetu tumemaliza Zahanati sita na Kituo cha Afya kimoja, lakini hatuna watumishi hata mmoja kwa ajili ya kuwahudumia wananchi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, unapokea taarifa?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa hii ya Mbunge mwenzangu kwa sababu ndio Mbunge ambaye tunatoka kwenye Wilaya moja. Wilaya ya Kahama ina Majimbo matatu kwa maana ya Ushetu, Msalala na Kahama Mjini. Kama ninavyosema, tuna watumishi 10 tu wa TAKUKURU na watumishi hao 10 wa TAKUKURU ni wanne tu ambao wanafanya shughuli hizo za tafiti na katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Jimbo la Msalala, Mama Samia Suluhu Hassan ameweza kutupatia kwenye bajeti ya 2021 zaidi ya takribani shilingi bilioni 24 kwenye miradi ya afya, kwenye miradi ya umeme na kwenye miradi ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo kwenye Jimbo la Mheshimiwa Cherehani Ushetu nako fedha zimekwenda nyingi. Ni saa ngapi sasa hao wafanyakazi wanne tu wa TAKUKURU wataweza kusimamia miradi ile? Nimemwona Mkurugenzi wa TAKUKURU hapa ndugu yangu Salum yuko hapa, Mheshimiwa Waziri tuongezeeni na ikiwezekana mtuletee Ofisi kwenye Halmashauri zetu. Idadi hii ya watu 10 ambayo imetajwa hapa ndiyo idadi sahihi ya kwenye kila Halmashauri, lakini sisi tutaangalia Halmashauri tatu, zote tuna wafanyakazi 10 tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, atuongezee na ikiwezekana atuwekee ofisi za TAKUKURU kwenye kila Halmashauri; kwa maana ya Halmashauri yangu ya Msalala, Halmashauri ya Ushetu na waliopo wabaki Halmashauri ya Kahama Mji. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi kwa mchango wako. Nilimwita Mheshimiwa Nicodemas…

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Nilimwita Mheshimiwa Nicodemas Henry Maganga wakati huo wafuatao wanajiandaa: Mheshimiwa Bahati Keneth Ndingo, Mheshimiwa Halima Mdee, Mheshimiwa Amandus Julius Chinguile.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia hotuba ya Ofisi ya Rais, Utumishi na Utawala Bora. Awali ya yote napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu tena kwa siku ya leo kuweza kusimama mahali hapa kuwawakilisha wananchi wangu wa Jimbo la Mbogwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye hoja kulingana na muda. Wilaya yangu ya Mbogwe ina upungufu wa watumishi 467 kwenye nyanja mbalimbali; walimu pamoja na kitengo cha afya. Namwomba Waziri wa Utumishi na Utawala Bora aangalie Wilaya yangu ili kusudi iweze kupata watumishi 467 ili wananchi wangu wa Mbogwe waweze kuhudumiwa kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo zipo changamoto zinazowakabili watumishi hasa kwenye upande wa afya. Unakuta mgonjwa amekuja huyu mtumishi anakwenda kumhudumia lakini hakuna vifaa tiba. Daktari anakutana na mgonjwa ambaye ameumia kwa ajali mfano ya bodaboda, hana vitendea kazi. Kwa kuwa, Wizara hii inahusika na watumishi, ni vyema Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri mtenge muda wa kuwaona kwanza watumishi hawa matatizo yao. Ni shida gani zinazowakabili katika upande wa utumishi wao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo changamoto nyingi kwa watumishi. Mimi nimekaa nao, nimekuwa mwanachama sana wa kupiga nao story watumishi ili kujua shida gani inayoweza kuwakabili kwenye kazi zao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala la uhamisho, Mheshimiwa Tabasam pale amezungumza japokuwa watu wameshindwa kumwelewa vizuri. Naomba nifafanue hiyo hoja. Suala la ndoa ni amri kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwamba kila mtu atakuwa na mwenzake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kumekuwa na tabia, mtu anapata uhamisho kwenda Mtwara kutoka kwa mfano, Bukoba; ina maana ndoa hiyo inakuwa ya ku-scratch scratch, hakuna ndoa pale tena. Maana katika taratibu za ajira jinsi zinavyotolewa hizi ruhusa ya kwenda kusalimia watu wako nyumbani ni kwa mwaka sijui siku 14 na vile vile akitaka mtu aende sasa kwenye familia yake, Serikali inatoa nauli tu bila kuangalia kwamba huyu mtu anaishi Mtwara, anatakiwa alale Dar es Salaam kesho yake ili aamkie kwenda kwenye familia yake, kunakuwa hakuna bajeti kama hiyo. Kwa hiyo, hilo Serikali iliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala moja la hawa madereva. Mwaka jana wakati naingia humu nilizungumzia habari ya madereva. Katika sekta hii ya utumishi, madereva wanapata taabu sana. Ajali hazitaisha bila kuwasemea hawa watu. Kuna baadhi hata ya Waheshimiwa, wanakaa na madereva hawasemeshani ndani ya gari. Lililopo, dereva hapo anakuwa anafikiria tu jinsi gani ampige chini bosi wake ili kusudi maisha haya yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unakuta dereva halipwi mshahara, hana mkataba wa kufanya kazi, anavyopelekwa dereva, yaani bora hata kuku au ng’ombe, yaani anaburuzwa tu. Unakuta Mbunge ametoka hata Bungeni bila kujua dereva huyu amekula, wala nini; kana kwamba yeye sio binadamu, ni kama anatumia remote. Inaniuma sana kwa kuwa maisha haya ya udereva na mimi nilishayaishi. Kwa hiyo, hii sekta sasa ione sababu, na Mheshimiwa Waziri…(Makofi) [Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

MWENYEKITI: Mheshimiwa, unao mfano wa Mbunge ambaye anafanya hivi? Maana umetaja Wabunge hapa.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hapana, siyo vizuri kumtaja mtu. Watajijua tu wale wenye roho mbaya, wataweza kuacha.

MWENYEKITI: Basi ifute hiyo; kwa upande wa Wabunge, ifute hiyo.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, haya, naifuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee tu kwa kuwatetea hawa madereva. Kuna dada yangu pale aliongelea suala la madereva wale wanaosafiri na magari makubwa (transit), wanapata taabu sana kwenye nchi hii, lakini hawa madereva wana chama na wana uongozi wao wa Kitaifa, nimekaa nao. Ukiwasikiliza madai yao ni ya msingi. Wanapopewa malori siku ya kuachishwa kazi hawaandaliwi kwamba lini mkataba wa ajira utasitishwa. Hawa madereva wana familia zao, wanalisha kupitia haya magari, lakini pale anapomdai tajiri mshahara wake, tajiri anamsingizia lose pamoja na mambo mengine ili kuweza kumfukuza huyu dereva. Kwa hiyo, kwenye sekta hii haijakaa vizuri, naomba Wizara hii kwa vile inahusika, iweze kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine, kwenye Halmashauri yangu nina wasomi wengi sana, hawajapata ajira. Mheshimiwa Lusinde amezungumza. Naomba sasa kama kuna uwezekano tufumue huu mfumo wa kuajiri kwa computer, maana computer hazichukui watu wa kijijini. Kuna walimu wengi vyeti vinaoza majumbani, hawapati ajira. Kuna madaktari wengi wamesoma, wako vijijini, wengine walishakata hata tamaa kabisa kuingia kwenye online hizi, maana hata kama uki-apply haupati kazi unakuta imefyatua tu watu wengine wa Dar es Salaam, Arusha lakini Mbogwe haionekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwa ushauri wangu, hizi ajira ziwe zinatolewa kila Halmashauri ili wasomi hawa tuliowasomesha kama Serikali waweze kuajiriwa. Kama kuna ugumu sana, Serikali muwe wawazi tu, kama nafasi zilishajaa kabisa hakuna haja hata ya kuwalazimisha watu kusoma sasa. Maana unamlazimisha mtoto anapomaliza Darasa la Saba akasome, atafute ajira, halafu kazi zinakuwa hazipatikani. Watu hawa wanakuwa hawajui kusoma, hawajui kulima na kufanya kazi zile nyingine ngumu. Wamefanya kazi yao ya kusoma na wamehitimu vizuri, lakini ajira hazipatikani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iliangalie suala hili la kuajiri watu upya. Wapo watu wanajitolea miaka na miaka, wengine wana miaka hadi 15 wanajitolea kwenye mashule kufundisha pamoja na kufanya mambo mengine, lakini hawapati ajira kabisa. Kwa hiyo, namwomba Waziri ajaribu kuliangalia hili suala ili kwenye Halmashauri zetu katika hizi ajira ulizozitangaza 3,200…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante.

MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: …ziweze kupatiwa ufumbuzi, kila Halmashauri at least watoke watu mia mbili mia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. IDD K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuniweesha kunipa afya njema leo kusimama katika Bunge hili Tukufu na mimi leo kuchangia kwenye hotuba ya Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Mama Daktari Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya kwa nchi yetu hii ya Tanzania. Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitampongeza Mheshimiwa Mama Daktari Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi ambazo ametutunuku wana Msalala. Mama Daktari Samia Suluhu Hassan ametupatia fedha nyingi katika miradi mbalimbali ikiwemo Huduma za Afya, barabara, umeme, maji, na maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukianza na afya. Mama Samia Suluhu Hassan ametupatia fedha ambazo zimetupelekea kujenga kituo cha afya katika kata ya isaka kiasi cha shilingi milioni 500 hajaishia hapo akatuongeza fedha nyingine kujenga Kituo cha Afya Kata ya Morogoro milioni 500, hajaishia hapo ametupatia fedha nyingine kujenga Kituo cha Afya Kata ya Burige milioni 500, hajaishia hapo akatupatia fedha nyingine milioni 400 kujenga Kituo cha Afya Kata ya Segese. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulikuwa na uhaba wa zahanati katika maeneo mbalimbali ya maboma lakini Mama Daktari Samia Suluhu Hassan ametupatia fedha kwa ajili ya kukamilisha maboma zaidi ya 18 ya zahanati ambayo yote yamekamilika mpaka sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambambamba na hilo, ili kuhakikisha ya kwamba tunaondoa upungufu wa watumishi katika maeneo hayo Mama Daktari Samia Suluhu Hassan ametupatia fedha ambayzo fedha hizo tumeenda kujenga chuo cha nursing na sasa kipo katika hatua ya mwisho ili kianze kutoa hudumahajaishia hapo ametupatia fedha kwenye sekta ya barabara. Mambo mengi sana kwa niaba ya wana Msalala nichukue fursa hii kumpongeza Mama Daktari Samia Suluhu Hassan kwa wema aliotutendea sisi wana Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya lakini kwa hotuba hii ya leo ambayo amewasilisha hapa bungeni. Katika hotuba hii ya Waziri Mkuu imeanisha kwamba ataenda kuboresha miundombinu ya barabara na niseme katika suala langu la barabara hasa niliouliza hapa asubuhi kwenye swali la nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna fedha ambazo zimetolewa kwa ajili ya ujenzi wa barabara inayotoka Buliankhulu inaenda mpaka Kahama lakini pia barabara hiyo inaunganisha kutoka Ilogi kwenda mpaka Geita lakini hivyohivyo inatoka hapo inaenda Nyang’wale inaenda mpaka kuunganisha daraja ambalo linajengwa la Kigogo Busisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii na leo niizungumzie kwa uchungu mkubwa sana kwa sababu Mheshimiwa Naibu Waziri leo wakati ananipa majibu yake pia alinipa majibu ambayo hayakuridhisha kabisa. Fedha hizi Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan ameidhinisha kiasi cha Shilingi dola milioni 40, takribani bilioni karibia bilioni 100 kwa ajili ya ujenzi wa barabara hii na fedha hii ipo na toka mwaka jana barabara hii ilikuwa ianze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na kuwa na milolongo mingi ya manunuzi, vikao vingi ambavyo havikamilishi ajenda zao bado mpaka tunavyozungumza hivi hakuna mpaka leo tunaambiwa bado makabrasha yanaandaliwa ili mkandarasi watangaze tenda hiyo. Sasa niseme fedha hii tumepatiwa na Mgodi wa Bulyankhulu na niwapongeze sana mgodi wa Bulyankhulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahusiano ya sisi tunaoishi karibu na migodi na wananchi yalikuwa ni mabaya mno lakini niwapongeze sana Mgodi wa Barrick na hasa kupitia maafisa wao wa mahusiano akiwemo Agapiti anafanya kazi kubwa sana. Wameona kuna haja ya kutupa fedha ili tujenge barabara hii kwa kiwango cha lami ili tuondoe vumbi ambayo itapitika kila leo na makinikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wanaathirika na vumbi, wameamua kutenga fedha kwa ajili ya kujenga barabara hii, lakini leo kumegeuka sasa Wizara ya Ujenzi kumegeuka kuwa ni sehemu ya kutafuta sijui ni nini lakini kila siku ni vikao wameanza vikao vya kwanza tumekaa kila kata tukamaliza wakaja wakafanya tathmini wamemaliza, wamerudi tena wanasema wanataka warudie wafanye review ya upembuzi yakinifu wamemaliza na wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii hawataki kutangaza Barabara hii na fedha ipo, mgodi huo madini yakipotea tutapata wapi fedha? Tumepewa fedha za wahisani tujenge barabara Mheshimiwa Naibu Waziri unakuja kusimama hapa majibu rahisi kabisa mpaka leo hamjatangaza nini ambacho kimewafanya ninyi msitangaze barabara hii? Fedha zipo siyo kwamba hazipo hata leo mkileta certificate wanalipa wale watu. Fedha zipo cash kwa nini hamjengi Barabara hii wananchi wanaendelea kuumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Barabara hii ni nguzo ya uchumi katika kuunganisha Geita toka Mkoa wa Geita mpaka shinyanga lakini leo nimezungumza hapa nikasema kahama ndio kitovu cha uchumi kanda ya ziwa. Unapozungumzia kanda ya ziwa huwezi kuiacha Kahama. Kuna wafanyabiashara wakubwa wanahitaji kusafirisha watu wanahitaji kuleta mali kutoka geita wanahitajikuleta mali kutoka Kagera na maeneo mengine. Barabara hii fedha zipo leo mtatuambia nini nani kachelewesha? Leo mnaniambia dakika ya mwisho naulizia wanabadilishana kukaa vikao naambiwa leo wameitana tena wanataka kwenda kukaa Dar es salaam kikao cha nini? kila siku mnakaa vikao kama vikao vya harusi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inauma, vikao vimekuwa ni vingi sana. Vikao vile vinatumia posho fedha ile itajenga Barabara lini? Fedha ipo wananchi wanaumia niombe Mheshimiwa Waziri Mkuu atakaposimama hapa kufanya windup ya hili atueleze ni lini hasa barabara hii itaanza kujengwa kwa sababu fedha zipo hakuna kinachoshindikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inauma sana leo nimezungumza kwa uchungu sana kwa sababu ninaona kuna uzembe mkubwa unafanyika kwenye maeneo haya hasa Wizara ya Ujenzi. Barabara nyingi ukiangalia, kuna barabara zinachelewa kujengwa na ukiuliza tatizo ni nini wanakuambia tatizo ni eidha ni hatua za manunuzi kwa nini tusizipitie upya hizi hatua za manunuzi? Ukiuliza unaambiwa bado kuna changamoto ya kupata tax exemption kwa nini hawa watu wa TRA wasikae pamoja na watu wa ujenzi wakaorodhesha barabara zote kama kikwazo kama ndio kupewa msamaha wa kodi wangalie ni namna gani wanaweza wakafanya ili kutoa msamaha wa kodi haraka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inauma sana kuona watendaji wanakuwa wazembe kiasi hiki. Mheshimiwa Rais anapambana kutafuta fedha, anaenda nje kutafuta fedha anatuletea fedha, anajitoa kuzungumza na wahisani mbalimbali leo watu wanakuja wanataka kutusaidia lakini watendaji wanamwangusha Mheshimiwa Rais. Ni katika shilingi nitakapokuja kuchangia Wizara nitashika mshahara wa Mheshimiwa Waziri mpaka atuambie ni lini barabara hii itaanza ujenzi kwa sababu fedha hizo tunazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze pia kwenye suala zima la TARURA amezungumza Mbunge mwenzangu hapa. Wilaya ya Kahama ndio wilaya kubwa inawezekana kuliko wilaya zote hapa Tanzania. Ukiangalia Mkoa wa Shinyanga ndio unaweza kuwa ni mkoa mkubwa lakini una wilaya chache kuliko zote hapa Tanzania. Mkoa wa Shinyanga una wilaya tatu tu lakini una halmashauri sita, sasa niombe TRA wamefungua Mkoa wa Kikodi Kahama, watu wa amdini wamefungua Mkoa wa Kimadini Kahama, niombe kwa nini hawa watu wa TARURA nao wasifungue Mkoa wa Ki-TARURA Kahama? Lakini pia tulikuwa na hawa Mameneja kwenye halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Kahama ina vijiji zaidi ya mia tatu na ishirini na kitu, leo kama Mkuu wa Wilaya akianza kutembelea kila Kijiji maana yake ni kwamba mwaka mzima yeye asifanye shughuli nyingine wala kwenda likizo anatembelea tu vijiji. Kwa nini hawa Mameneja wasirudishwe ili waweze kutoa huduma?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mvua zinaendelea kunyesha tunapokea malalamiko kwenye maeneo yale utaona barabara zinakatika, watu wanataka kurekebisha barabara lakini ukiuliza hatua za manunuzi hivi haya manunuzi hamuwezi mkayaleta hapa tukayapitia tukaona njia rahisi ya kurekebisha? Leo utaanza kuona tunapitisha bajeti mwezi wa saba mwezi saba akaunti zimefungwa mfumo bado tunaenda tunatangaza tenda, tunatangaza tenda hatua za manunuzi, manunuzi, manunuzi, mpaka mkandarasi anaenda site mwezi wa pili mvua zinanyesha barabara haitengenezwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Mama Dkt. Samia Suluhu Hassan anatafuta fedha nyingi anatuletea, changamoto siyo fedha kwenye maeneo yetu kwa sasa fedha zipo lakini changamoto utaambiwa tulitangaza barabara hii mkandarasi hakupatikana, hakupatikana alienda wapi? Wanasema tumetangaza barabara hii hatua za manunuzi bado, bado kivipi? Wakati meza zipo? Niombe sana Wizara ya TAMISEMI hebu oneni namna ya kuweza kuona namna ya kurudisha mfumo ambao uliokuwepo wa Mameneja Wilaya ya Kahama ni wilaya kubwa mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyohivyo niendelee kuomba ikiwezekana basi tuone namna ya kugawa utawala mtuongezee hizi halmashauri, Halmashauri yangu ya Msalala, Halmashauri ya Usheto na Halamashauri ya Manispaa ya Kahama hizi zote zinajitegemea kiuchumi na uchumi wao ni mzuri, kwa nini tusipatiwe wilaya kila sehemu tukajitegemea? Kwa sababu halmashauri yangu ni halmashauri lakini ukilinganisha na wilaya zingine inawezekana kiuchumi Halmashauri ya Wilaya ya Msalala ikawa iko vizuri kuliko wilaya zingine ambazo zinaendelea hasa niazoziona za Jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimezungumza sana kwenye suala zima la barabara naumia sana, kwenye umeme nitakuja nizungumze kwenye Wizara ya umeme lakini niombe hii barabara ni changamoto kubwa sana na narudia tena kwa sababu ni barabara ambayo kuna uzembe na ikiwezekama watu wawajibike kwenye hili, nani amekwamisha? Nani kashikilia? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inaniumiza sana kuona fedha tunazo kwenye maeneo mengine wanalia kila siku Mheshimiwa Naibu Waziri anatuambia ikipatikana fedha Serikali itajenga sasa fedha imepatikana kwa nini hamjengi? Kama fedha ikipatikana leo ipo Mheshimiwa Naibu Waziri na Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii na Katibu Mkuu niwaombe sana punguzeni vikao. Ikiwezekana CAG nimuombe kwenye ripoti inayokuja achunguze hivyo vikao vinavyo kaa kaa hivyo vikao vinatumia fedha kutoka mfuko gani? Kwa sababu vikao vimekuwa vingi haviishi kutangaza barabara mbona barabara zingine hazina vikao vingi kama hii barabara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunaozalisha dhahabu ukiangalia mgodi wa Buliankhulu na jimbo langu la Msalala ndio jimbo ambalo linachangia kwa kiasi kikubwa sana kwenye mfuko wa taifa. Leo hii utaona kwenye wizara ya madini tunalipa reality asilimia saba na niendelee kuomba Mheshimiwa Waziri yupo hapa ananisikia Mheshimiwa Waziri Mkuu nikuombe sana watu tunaotoka kwenye maeneo ya madini maisha yetu ni duni, hayafanani na vile ambavyo tunazalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe ikiwezekana kwenye asilimia saba ambayo tunalipa mrabaha asilimia saba ambayo makampuni yanalipa mrabaha niombe asilimia mbili iweze kubaki kwenye maeneo hayo ili tuweze kujenga miundombinu yetu wenyewe kwenye maeneo yale bila kutegemea fedha kutoka Serikali kuu, uwezo huo tunao kwa sababu fedha zipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeongea kwa uchungu sana nafikiri nisiharibu niishie hapo lakini niombe na niombe nitashika shilingi kama barabara hii haitaanza kujengwa kwa sababu fedha zipo, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii ili leo niweze kuchangia kwenye bajeti hii ya Wizara ya Madini.

Kwanza nianze kabisa kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kunipa afya njema na kuniwezesha kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kujadili hotuba ya bajeti ya leo. Vile vile, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitapeleka shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika nchi hii lakini hasa katika Sekta ya Madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Mheshimiwa Rais, Mama yangu Samia Suluhu Hassan ametuheshimisha wachimbaji wadogo wadogo kwenye Nchi hii ya Tanzania. Historia inaonesha katika watu waliokuwa wakidharaurika katika nchi hii ilikuwa ni wachimbaji. Hata hivyo, leo hii unapozungumzia habari ya wachimbaji wadogo wadogo unaona kabisa ni watu wenye heshima zao, wanaweza kwenda wakakaa sehemu wakaonekana ni watu wenye heshima, wakawekeza, wanafanya mambo yao kisomi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Dkt. Biteko anafanya kazi kubwa sana. Asubuhi hapa nimemsikia Mbunge mwenzangu akishauri Serikali waone kuwa na mpango wa kuweza kumpatia certificate, lakini nasema kama vyama vya wachimbaji vinanisikia huko viliko kwa maana ya FEMATA, TAWOMA na nimeona hapa chama kimoja cha wachimbaji vijana kiko hapa, wanafanya kazi kubwa kwa maana ya kusimamia wachimbaji vijana katika Sekta ya Madini. Kuna haja kubwa ya kumjengea sanamu Mheshimiwa Dkt. Dotto Biteko, ametufanyia kazi kubwa sana kwenye Wizara hii ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapozungumza mchimbaji mdogo mdogo aliyekuwa akichangia asilimia 20 na sasa asilimia 40, sio miujiza. Ni mipango mzuri, mikakati mizuri inayosimamiwa na Dkt. Dotto Biteko chini ya usimamizi wa Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile, nimpongeze hata Naibu wake Waziri na niwe wazi, katika Wizara ya Madini, Mheshimiwa Rais amefanya uchaguzi mzuri kabisa. Ukienda kwa Mheshimiwa Waziri ni msikivu na mnyenyekevu, ukienda kwa Naibu Waziri naye ni msikivu na mnyenyekevu, ukienda kwa Katibu Mkuu ndio usiseme meno 32 wakati wote sijui anachukia saa ngapi Mheshimiwa Katibu Mkuu wa Wizara hii. Ukienda kwa Mtendaji Mkuu wa Tume, yuko vizuri, Kamishina naye yuko vizuri. Hiyo inatufanya sisi wachimbaji wadogo wdogo kuwa na moyo wa kuwekeza na kuonesha kwamba Serikali kweli inatujali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze sana, leo hii tunazungumzia habari ya STAMICO. Utaona kabisa STAMICO hapo mwanzoni ilivyokuwa na sasa ilipo inafanya kazi nzuri sana. Wameanzisha miradi mbalimbali na leo hii wanazungumzia habari ya kumuunga mkono Mheshimiwa Rais katika kutunza mazingira.

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kassim kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Mwita Waitara.

TAARIFA

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Kassim kwamba kwa wema wa Mheshimiwa Dkt. Biteko na mwenzake Mheshimiwa Kiruswa, leo ninapozungumza wananchi wa Nyamongo hawanywi maji ya sumu tena, wanakunywa maji safi ya bomba. Hongera sana Mheshimiwa Dkt. Biteko kwa kazi nzuri. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kassim taarifa unaipokea?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii mimi naipokea kwa mikono yote miwili, Dkt. Biteko anafanya kazi nzuri sana, hata siyo Nyamongo tu nimpe taarifa Mheshimiwa Mwita Waitara ukija Kata ya Bulyanhulu na Mheshimiwa Amar yupo pale Nyang’wale utaona fedha nyingi ya CSR ambayo inatumika kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii Msalala tunazungumzia tumemaliza zahanati 34 kwa mpigo, yote haya ni matunda ya Mama Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Dkt. Biteko.

Tunazungumzia habari ya vituo vya afya hapa juzi nilizungumzia habari ya lami tayari wako site wanaendelea kumalizia taratibu za kuanza ujenzi wa lami kilomita 76 kiasi cha Shilingi Dola Milioni 40 yote haya ni matunda mazuri ya Mheshimiwa Dkt. Biteko chini ya uangalizi wa Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu mpendwa kipenzi cha Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninataka kuzungumzia hapa, naomba nishauri tuna Vyama vya Wachimbaji hivi ambavyo kazi yao ni kusaidia wachimbaji, niombe sana STAMICO na Mheshimiwa Waziri niombe sana vyama hivi hebu oneni namna ya kuvisaidia viweze kuwasaidia kwa kazi nzuri mnayoifanya. Leo hii tunazungumzia habari ya uchimbaji kuna wachimbaji vijana wapo lakini ukiwaangalia kutafuta nani anawasaidia vijana hawa huoni na ndiyo maana umeona kuna taasisi imeanzishwa kwa ajili ya kuwasaidia vijana. Leo hii utaona kuna watu wanauza madila nani anawasaidia madila leo hii ukienda utaona kuna watu wana-plant nani anawasaidia plant? Vyama hivi ni lazima vikae chini vione namna ya kuunda reform, waunde umoja na umoja huu utasaidia katika kuhakikisha kwamba inaisaidia Wizara ili iweze kufanya vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumzie habari ya wachimbaji kwenye Jimbo langu la Msalala, amezungumza Mheshimiwa Nusrat Hanje nimuombe Mheshimiwa January Makamba na hili nitalizungumzia tunavyokuja kuzungumzia suala la umeme, changamoto kubwa ya umeme inakwamisha shughuli za madini katika maeneo yetu, hilo nitalizungumzia nitakapokuja kuchangia kwenye suala zima la REA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Mheshimiwa Waziri wachimbaji wadogo wadogo hatuendelei kwa sababu ya kukosa mikopo. Leo katika hotuba yako nimeisikiliza vizuri, tumepongeza hapa mabenki yamefanya kazi kubwa ya kukopesha wachimbaji wadogowadogo, lakini nataka nikwambie inawezekana takwimu hizi za ukopeshaji haya mabenki wanakopesha wachimbaji wakubwa, lakini bado kwa wachimbaji wadogowadogo kupitia imani ambayo wewe mwenyewe umeijenga bado hawakopesheki, hakuna benki ambayo inakopesha mchimbaji mdogomdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuomba Mheshimiwa Waziri na niombe BOT, tumeona BOT imetoa fedha nyingi zaidi ya Bilioni kadhaa kuyapa mabenki ili mabenki haya yaweze kuwakopesha wachimbaji wadogowadogo, lakini unapoenda mchimbaji mdogomdogo kukopa fedha kwenye mabenki haya haukopesheki mpaka wanakuomba aidha ufungue biashara nyingine au uwe na dhamana nyingine, wakukopeshe fedha zile kupitia mgongo wa biashara nyingine na siyo madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii kama wachimbaji wadogowadogo inapelekea wanakosa mitaji ya kuendeleza shughuli za uchimbaji leo hii utaona, akija hapa Mzungu na briefcase akapeleka plan kwenye mabenki haya anapewa mkopo lakini akienda ngozi nyeusi kwenda kuomba mkopo hapewi, mabenki haya yatueleze kama yana ushahidi yamempatia nani mchimbaji mdogomdogo watueleze waweke ushahidi hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ni-declare interest, mimi ni mchimbaji ninachokisema hiki ninauhakika nacho, hakuna mchimbaji mdogomdogo ambaye kakopeshwa fedha na mabenki haya. Sasa kuna haja ya kukaa na mabenki haya niiombe BOT ikae na mabenki haya, kwanza ukiona BOT inawapa mikopo mabenki haya kwa asilimia ndogo sana, asilimia tisa na lengo la mikopo hii ni kutukopesha wachimbaji wadogowadogo lakini utaona wachimbaji wadogowadogo bado hawaaminiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na Mheshimiwa Waziri kufanya kazi kubwa ya kuwapatia leseni wachimbaji wadogowadogo lakini bado leseni zao hazitumiki kama kigezo cha wao kupatiwa mikopo, kwa hiyo niombe sana na niombe Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ananisikia waweke mkakati wa kuhakikisha kwamba wanakopesha wachimbaji wadogowadogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye bajeti hii hapo zamani wachimbaji tulikuwa tunakopeshwa walikuwa wanakopeshwa wote kwa maana ya mikopo na baadae Serikali iliondoa, sasa wewe mwenyewe umetueleza Mheshimiwa Waziri kwamba wachimbaji wa sasa ni wa kisasa, hebu nikuombe sasa kwa sababu tayari wachimbaji wa sasa wako kwenye reform, mikopo iliyokuwa ikikopeshwa iweze kurudi sasa ili iwasaidie wachimbaji kuelekeza kuchimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Nyongo amezungumza hapa Habari ya GST. GST inaendelea kufanya vizuri, niombe waendelee kufanya kazi kubwa kuzunguka maeneo yetu, waweze kuandaa ripoti wafanye reserve estimate, wawapatie wachimbaji wadogowadogo na Wizara mkitupatia hiyo mikopo wachimbaji wadogowadogo maana yake ni kwamba itaenda kusaidia katika kuhakikisha kwamba sekta yako Mheshimiwa Waziri inakua kwa kasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, amezungumzia habari ya ufungaji migodi hapa Mbunge mwenzangu, Mheshimiwa Waziri nikuombe sana pale Kahama tuna mgodi wa Buzwagi ambao umefungwa, plan iliyopo pale ni kwenda kufanya kuwa eneo la economic zone sikatai ni wazo zuri, lakini niendelee kuomba sana kwa sababu Kahama nzima inategemea uchumi wa madini na leseni ile kwa sababu hawa watu wanaenda kuiachia, na kwa kuwa wanaenda kuiachia bado ina madini ambayo wakipewa wachimbaji wadogowadogo wanaweza wakapata fedha kupitia maeneo yale. Ninaomba Mheshimiwa Waziri ikiwezekana ikikupendeza hebu gaweni ile leseni sasa kwa wachimbaji wadogowadogo pale Buzwagi ili iweze kukuza uchumi wa Kahama Mjini na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie habari ya GST na STAMICO, leo hii utaona GST katika maeneo haya wanazo maabara za upimaji madini katika Jiji la Dodoma na niwapongeze Mheshimiwa Waziri wameenda kufungua maabara nyingine Geita. Sasa maeneo mengine mengi Mheshimiwa Waziri kama Chunya, Kahama ambayo ndiyo maeneo ambayo yanazalisha dhahabu kwa wingi ninaomba sana Mheshimiwa Waziri uweze kuanzisha maabara kubwa kwenye maeneo haya ili tuwarahisishie wachimbaji wadogowadogo wanapoweza kuchimba madini yao waende wakapime sampuli zao kwenye maabara za Serikali ambazo zitawapa uhakika, kwa sababu wachimbaji wengi wanafilisika sana kwa sababu ya vipimo vya maabara hizi zilizoko mitaani ambazo hazina uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba sana watu wa GST..

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kassim muda wako umeisha.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana na ninaunga hoja kwa asilimia 100, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia fursa hii nami leo kuchangia. Kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, hasa kwenye sekta hii ya afya. Nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, nampongeza pia Naibu Waziri Mheshimiwa Dkt. Mollel kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Niseme tu kwamba, kwa kweli Waziri ana Naibu Waziri ambaye ni mchapakazi sana. Mimi nitakuwa ni mfano wa Wabunge ambao nimeshuhudia kazi kubwa ambayo anaifanya Naibu Waziri. Hafanyi yeye, ni kwa sababu Waziri anamtuma. Kwa hiyo, ni mtiifu kwake, anatii maelekezo yake na anakuja kutusaidia kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimefanya kazi ya ziara na Mheshimiwa Dkt. Mollel kwenye Jimbo la Msalala tukizungukia vituo vya afya na zahanati mpaka saa nne za usiku, na wakati huo tunafanya ziara hiyo toka asubuhi mpaka jioni alikuwa hajala, anakula korosho na maji. Ni huyu anajali afya za Watanzania, na hata sisi Wabunge anatusikiliza na kutufanyia kazi kubwa kwenye maeneo yetu hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza sana Mheshimiwa Katibu Mkuu na Naibu wake, dada yangu Grace, naye pia anafanya kazi kubwa sana. Nimekuwa nikikutana naye mara kwa mara akihangaika kutembelea miundombinu ya afya katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa, nampongeza Mheshimiwa Daktari Mama Samia Suluhu Hassan kwa wema wake wa kututendea sisi Watanzania katika sekta hii ya afya. Katika Jimbo la Msalala mimi naweza nikawa ni Mbunge ambaye nimepata bahati sana ya kupata fedha nyingi ambazo zinaenda kwenye vituo vya afya, kwenye zahanati, na ununuzi wa vifaa tiba kwenye maeneo hayo. Mama Samia Suluhu Hassan ametoa fedha, tumejenga, tumemaliza kituo cha afya na Mheshimiwa Dkt. Mollel nafikiri alifika baada ya kutumwa na Waziri, akakitembelea Kituo cha Afya Isaka, kimekamilika, kimeanza kutoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo hivyo, tumekamilisha Kituo cha Afya Mwalugulu kinatoa huduma, tumekamilisha Kituo cha Afya Bulige kinaendelea kwenye ukamilishaji, Segese na chenyewe kipo kwenye hatua ya mwisho, Mwalugulu tayari, kwa hiyo, utaona zaidi ya vituo vinne vya afya vyote vinakamilika. Niendelee kuwapongeza sana wadau wakubwa, Barrick ambao kimsingi wameunga jitihada za Mheshimiwa Rais katika kukamilisha zahanati mbalimbali. Wametupatia fedha, tumeweza kukamilisha zahanati 34 kwa mpigo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika Jimbo la Msalala tuna vijiji 92 na tunavyozungumza hivi, matarajio yetu mpaka sasa tumebakiza maboma zaidi ya kumi na kitu tukamilishe idadi ya kila Kijiji kuwa na zahanati; na vituo vya afya vinane. Hapa tunapozungumza Mheshimiwa Waziri tunapata fedha nyingine, mmetuletea tena, tunaenda kuanza ujenzi wa vituo vya afya Kata ya Mwanase na Kata ya Busangi. Kwa hiyo, utaona zaidi ya zahanati 92 kwenye vijiji hivyo, utaona vituo vya afya vinaenda kuwa zaidi ya kumi, na pia kuna hospitali ya Wilaya ambayo na yenyewe tayari imekamilika, na niwapongeze sana. Nampongeza Mama Samia Suluhu Hassan, tayari ametuletea fedha kiasi cha Shilingi milioni 700 tunaendelea kumalizia majengo ya mama na mtoto, mmetuletea fedha tumejenga ICU, na mmetuletea vifaa vya ICU kwenye maeneo hayo. Kimsingi, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan katika Jimbo la Msalala, tunamwahidi 2025 kura zake nyingi za kutosha kabisa tutampigia kwa sababu katika sekta ya afya ameonesha ni namna gani anatujali Wana-Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haitoshi, kwa kuwa tumepata zahanati zote, tumepata Vituo vya Afya, lakini namshukuru pia Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, ametupatia fedha za kununua vifaa tiba zaidi ya Shilingi milioni 600. Tayari kwenye maeneo haya, tumepeleka baadhi ya vifaa tiba, lakini bado havitoshi. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii, chonde chonde, tunazo zahanati zimekamilika na hivi sasa bahati mbaya nyingine zimeanza kuota nyasi baada ya kukosa vifaa tiba. Fedha mliyotupatia ni kidogo sana, tumejaribu kuweka kwenye zahanati zaidi ya nne tu, lakini bado kuna zahanati zaidi ya 24 hazina vifaa tiba. Siyo vifaa tiba tu, hata watumishi wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo la Msalala, kuna upungufu mkubwa sana wa watumishi kwenye kada ya afya. Utaona kwa sasa tuna watumishi Zaidi ya 264, lakini tuna upungufu wa watumishi zaidi ya 500. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri atusaidie ili tuweze kupata watumishi, kwa sababu tumekamilisha maboma ya zahanati kwenye kila Kijiji, lakini changamoto iliyopo sasa hivi ni vifaa tiba na watumishi ambao wataenda kutusaidia katika kuhakikisha kwamba tunazifungua zahanati hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niliposema kwamba Mheshimiwa Naibu Waziri alifika na amezishuhudia zahanati hizo kwa macho yake zipo, na sasa kwa wananchi kila siku wanaenda kufanya kazi ya usafi kwenye maeneo yale wakisubiri vifaa tiba na watumishi. Mbali na hilo, nashukuru sana wadau wetu wa Barrick na Serikali, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuona umuhimu, na namna gani anaweza kukabiliana na upungufu wa watumishi, tayari ametupatia fedha, shilingi milioni 400, tumejenga Chuo cha Afya. Hicho Chuo cha Afya sasa kinaenda kukamilika. Namwomba Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mollel amefika alipomtuma, amekiona ni chuo cha kisasa, ni chuo kizuri. Sasa niwaomba waende kukifungua chuo hicho ili tuweze kusaidia upungufu wa watumishi kwenye maeneo yetu hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kuwapongeza sana Mheshimiwa Waziri, wametujali mno. Mheshimiwa Naibu Waziri nakupongeza mno, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan nakupongeza mno kwenye sekta ya afya. Niseme tu kwamba kumekuwa na changamoto, na hii siyo kubwa sana lakini ichukulieni kwa uzito wake. Amezungumza hapa Mbunge mwenzangu, kwenye baadhi ya vituo vya afya, kuna maduka ambayo yameanzishwa mle ndani. Ninapozungumzia maduka haya, nahusisha suala zima la dawa. Kumekuwa na maduka kwenye vituo vya afya, lakini maduka haya bado hayajaunganishwa na huduma hii ya NHIF.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto kubwa utakuta maduka haya bado usajili wake ni tofauti na zahanati ni tofauti. Mtu mwenye kadi ya NHIF anapoenda pale hapewi huduma kwenye duka lile kwa sababu bado halijaunganishwa. Hivyo hivyo maduka haya kwa sababu tumeyafungua kimkakati kuweza kuhakikisha dawa zinapatikana kwenye maeneo yale, tuwape uhuru wa kuweza kufanya biashara. Wanapouza, wanapata fedha zile kwenda kwa mshitiri kama alivyozungumza hapa Mbunge mwenzangu hapa Mheshimiwa Reuben, bado kuna changamoto kubwa sana ya hawa washitiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba mtoe vibali vya kwenye maduka haya yaweze kununua dawa kwa haraka zaidi kwa sababu fedha tunazo kwenye baadhi ya maeneo ya zahanati, lakini changamoto, wanapopeleka fedha zile aidha MSD au kwa mshitiri, dawa zinapokosekana, fedha zile zinabaki kule na wananchi wanaendelea kuumia. Toeni vibali, process hizi ni mpaka mtu atoke hapa aende mpaka kwa RAS Mkoani, wapate kibali ndiyo waje waanze kufanya utaratibu wa kununua dawa. Sasa naomba hebu toeni utaratibu wa namna gani maduka haya ambayo yamo kwenye vituo vya afya hivi, ili yanapotaka dawa yaweze kwenda kununua maeneo yoyote yanapohitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, sambamba na hilo, naomba tuweke mfumo mzuri kwenye vituo vyetu vya afya vya ukusanyaji mapato. Fedha nyingi zinapotea. Vile vile namwomba sana Mheshimiwa Waziri waone ni namna gani basi wanaweza kuviwezesha hivi vituo vya afya au zahanati viweze kuwa na vibali vya kuajiri kwa mkataba. Leo hii tunapozungumza hapa, ni kwamba ukiangalia Hospitali ya Bugarama kuna changamoto kubwa sana ya watumishi kwenye maeneo yale. Leo tumepatiwa fedha na Mgodi ya Bulyanhulu pale tumeweza kununua machine moja ya x-ray na utra-sound. Hata Mdhibiti Mkuu wa Serikali amezungumza, vifaa vile tumevinunua muda mrefu, tumevitunza pale, havina watumishi, havina wataalam wa kuviendesha, vimekaa pale. Naomba sana tuleteeni wataalam.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, wametuletea fedha nyingine tumenunua digital x-ray kwenye Kituo cha Afya cha Isaka, lakini bado na penyewe hatuna mtumishi. Sasa vifaa vya kisasa tunavyovileta kule, kama hatutatua changamoto ya ungufu wa wataalam kwenye maeneo yale, maana yake vifaa hivi vitakaa kwa muda mrefu na vitaharibika. Kwa hiyo, nawaomba sana, tuleteeni wataalam kwenye maeneo yale ili wananchi wetu sasa waweze kupata huduma kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki kuzungumzia habari ya ambulance kwa sababu mmeshatuahidi kwamba kila Jimbo tutapata ambulance. Kiu yetu ilikuwa ni ambulance. Kwa hiyo, ninaamini kabisa ambulance zikija, mimi Mbunge wa Msalala ndio nitapewa kipaumbele namba moja, ili nije nipokee ambulance hiyo ikafanye kazi kwenye maeneo yetu hayo ili kuhakikisha kazi kubwa kwenye huduma ya afya inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia la mwisho mtusaidie. Tunapozungumza habari ya huduma zinazotolewa kwenye vituo vyetu vya afya na zahanati, bado huduma haziridhishi kwenye maeneo yale, Mheshimiwa Dkt. Mollel aliona.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante kengele ya pili.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, endeleeni kuchapa kazi, tunawaamini. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa furasa na mimi leo kuchangia hotuba hii ya Wizara ya Nishati. Kwanza kabisa nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na mimi siku ya leo kuweza kuchangia bajeti hii ya nishati.

Mheshimiwa Spika, lakini pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya na hasa kutuwakilisha kwenda kushuhudia uapisho wa Rais wa Nchi ya Nigeria, vivyo hivyo kuendelea kutuwakilisha sana Watanzania katika mambo mbalimbali kimataifa. Nichukue fursa hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara, kaka yangu January Makamba. Kazi kubwa unaendelea kuifanya katika nchi hii kama alivyosema dada yangu Tauhida hapo. Sisi wananchi na hasa wananchi wa Jimbo la Msalala tunakuelewa. Tunakuelewa kwa ukarimu wako, tunakuelewa kwa uchapaji kazi wako; na wananchi wameniagiza kwa wema uliyowatendea baada ya wewe kufika katika Jimbo la Msalala kutuona, kututembelea na kutusikiliza maeneo mbalimbali yakiwemo maeneo ya wachimbaji wadogo wadogo kwenye maeneo yetu ya Msalala. Nimpongeze sana kwa kazi kubwa unayoendelea kuifanya lakini pia nimpongeze Naibu wako Waziri kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, nimpongeze Mkurugenzi Mkuu wa TANESCO, Mkurugenzi Mkuu wa REA kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii mimi nimesimama hapa kuwawakilisha wananchi wa Msalala kuhusiana na kero mbali mbali zinazohusu suala la umeme. Mheshimiwa Mbunge mwenzangu, Mheshimiwa Cherehani amezungumza asubuhi hapa kupongeza jitihada mbalimbali ambazo zinaendelea kwenye Wilaya yetu ya Kahama na hasa Mradi wa REA ambao unaendelea kutekelezwa kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikili ni kweli hapo mwanzoni palikuwa pamesuasua sana lakini sasahivi mkandarasi anaenda sawa sina haja ya kurudia kwa sababu Mheshimiwa Mbunge mwenzangu Cherehani amelizungumza jambo hili. Hata hivyo, niongezee hapo tu kidogo katika kumuhakikishia kwamba huyu mkandarasi anaenda ku-perform vizuri Mheshimiwa Waziri sisi wananchi wa Kahama, tunaomba huyu mkandarasi aweze kuongezewa zile kilomita mbili ili awe anamaliza kabisa ili kumuondolea usumbufu baadaye kuwa anarudi kuja kutekeleza zile kilomita mbili ambazo zimebaki. Kwa hiyo nikuombe sana muongezee mkataba. Sambamba na hilo kwa sababu ya vifaa niombe Mheshimiwa Waziri nendeni mkajaribu kuona utaratibu wa kumfungulia LC ili aweze kupata material kwa wakati, aweze kutimiza miradi hii kwa wakati ili wananchi wa Jimbo la Msalala na Wilaya ya Kahama waweze kunufaika na miradi hii ya umme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi amelizungumza Mbunge mwenzangu na mimi naomba nikazie. Wilaya ya Kahama ndiyo Wilaya ambayo inaongoza kwa kukusanya mapato yatokanayo na umeme kwenye Mkoa wa Shinyanga. Utaona makusanyo kwenye Mkoa wa Shinyanga ni takribani bilioni 16, lakini kiasi cha shilingi bilioni 13 zinatoka kwenye Wilaya ya Kahama. Ukitazama hapo utaona Wilaya ya Shinyanga Mjini ni bilioni mbili na Wilaya ya Kishapu ni kama bilioni moja na kitu. Kwa hiyo Wilaya ya Kahama ni eneo muhimu sana katika uwekezaji wa sekta ya umeme. Kwa hiyo nikuombe sana weka jicho lako katika kuwekeza kwenye Wilaya ya Kahama ikiwemo kuanzisha Mkoa wa ki-TANESCO.

Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia Mkoa wa Dar es salaam wameanzisha mikoa minne ya ki-TANESCO, sasa tunashindwa nini kuanzisha Mkoa wa ki-TANESCO katika Wilaya ya Kahama ili tuweze kuhakikisha ya kwamba tunasogeza huduma hii kwa haraka kwa wananchi wetu lakini pia tuone namna ya kuweza kusaidia watu ambao wanatoka kwenye maeneo mbalimbali kwenye maeneo yetu? Kwa hiyo nimuombe sana Mheshimiwa Waziri hili jambo la kuanzisha kwenye bajeti hii twende tukaanzishe Mkoa wa ki-TANESCO. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nimwambie Mheshimiwa Waziri, Meneja wa TANESCO Wilaya ya Kahama anafanya kazi kubwa sana. Wilaya ya Kahama ina halmashauri tatu, na ule ni sawa sawa na mkoa. Lakini pia kutokana na shughuli nyingi na maeneo mengi inanuwia vigumu meneja huyu kufika kwenye maeneo yale. Kwa hiyo niombe, baada ya kuanzishwa Mkoa wa ki-TANESCO katika maeneo yale, mkianzisha na ofisi kubwa za wilaya katika halmashauri zetu inatusadia sana kuhakikisha kwamba wananchi wanapata ile huduma kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, wafanye mazungumzo na hawa watu wa TRA. Wananchi wanalalamika kwamba kumekuwa na tabia sasa hivi, hasa ile kodi ya majengo ambayo inakatwa kwenye umeme. Kumekuwa na ulimbikizaji wa kodi ile haikatwi kwa wakati matokeo yake wananchi wetu ambao wana uchumi duni wa kununua umeme unakuta mtu anaenda kununua wa shilingi 10,000 wakati huo huo anadaiwa shilingi 6,000 au 10,000 hiyo, inakatwa na anapata unit ndogo. Kwa hiyo niombe mfanye coordination ya ninyi pamoja na TRA waweze kukata kodi ile mapema iwezekanavyo ili kuondoa mzigo mkubwa kwa wananchi wetu hawa kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimempongeza sana Mheshimiwa Waziri, nisisahau kumpongeza meneja wangu wa mkoa anafanya kazi kubwa sana Mkoa wa Shinyanga, nisisahau kumpongeza meneja wa kanda anafanya kazi kubwa sana. Bila ya hawa maendeleo huko kwetu, hasa katika sekta ya nishati yatashuka. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, siku zote huwa anazungumzia habari ya umeme, kwamba unapozungumzia umeme ni mambo matatu; uzalishaji, sina shaka na uzalishaji kwa sababu mambo mengi yanafanyika, anazindua miradi mingi, na juzi tumemuona Mheshimiwa Rais akiizindua Mradi wa Rusumo kazi kubwa inafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu usafilishaji sina shaka na usafilishaji, usambazaji sina shaka na usambazaji. Nataka nimuongezee hapo Mheshimiwa Waziri, aende akaanzishe suala jingine la ukusanyaji, TANESCO waweke mikakati mizuri ya kukusanya mapato kwenye maeneo yetu ili kuiwezesha TANESCO kuweza kusimama na kutengeneza faidi lakini pia kulipa madeni mbalimbali kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti hii Mheshimiwa Waziri amezungumza kwamba EWURA wametenga fedha kwa ajili ya kukopesha vijana wetu, kuanzisha vituo vya mafuta kwenye maeneo ambayo yana umbali mrefu kwenye vituo hivi vikubwa vya mafuta. Niombe kwenye maeneo hayo Mheshimiwa Waziri watafute namna ya kutoa semina nzuri kwa vijana wetu. Kuona ni namna gani wanaweza kupata taarifa sahihi ya namna gani wanaweza kupata mikopo hii ili na wao waweze kutumia fursa hii ya mikopo ya kuanzisha vituo vidogo vidogo vya mafuta kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuzungumza hayo kwa Mheshimiwa Waziri sasa naomba nizungumze suala moja zuri sana. Sitaki kuzungumza leo habari ya mafuta, na nimeona kwenye bajeti yake Mheshimiwa Waziri hapa amezungumzia habari nzuri ya mafuta. Mimi nataka leo nizungumze habari ya lubricant, kwa maana ya vilainishi.

Mheshimiwa Spika, biashara ya vilainishi kwenye nchi hii ni biashara kubwa sana. Kama Wizara hawataweka jicho katika kuhakikisha kwamba wanadhibiti uingizwaji wa lubricants, kwa maana ya vilainishi fake kwenye nchi hii itaendelea kutia hasara kubwa sana wananchi wetu katika maeneo haya. Mimi ni shuhuda nimeweza kuweka oil kwenye gari langu imeharibu engine.

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri, wananchi wengi wanaharibikiwa engine zao ni kwa sababu ya uingizwaji wa oil ambazo ni fake kwenye hii. Sasa niombe kwenye Wizara hii na EWURA, kupitia TBS waweke udhibiti mzuri ili kuhakikisha kwamba oil zinazoingia nchini ziwe ni oil ambazo zimethibitishwa na TBS kwa ajili ya kumlinda mtu anayekwenda kutumia. Tunaingia hasara kubwa sana ya gari zetu, tunaingia hasara kubwa sana kununua vilaishi hivi fake.

Mheshimiwa Spika, na hasa utaona kuna viwanda vingi bubu ambavyo vimeanzishwa kwenye maeneo hayo, wananunua oil ambazo ni chafu ni kwenye maeneo yale, wanazisafisha oil zile, wanaofanya package kwenye maeneo yale na matokeo yake tunaenda kuuziwa oil ya Total kumbe ni oil ya Total ambayo ni fake. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri waanzishe utaratibu wa kuwasajili wauza oil na vilainishi kwenye nchi hii ili kuwalinda wawekezaji wetu kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine nizungumze suala zima la namna ya kulinda biashara hii katika nchi hii. Katika makubaliano ya Mheshimiwa Waziri na nchi za East Africa, hasa Kenya, katika ushindani wa biashara hii utaona hapa Tanzania na Kenya kumekuwa na competition kubwa. Uanzishwaji wa viwanda vya vilainishi kwenye nchi imekuwa changamoto yake ni kubwa. kwa sababu ya kodi ambayo tunaweka kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, utaona wamekubaliana kwamba import duty ya lubricant katika nchi hii na katika East Africa iwe ni 10 percent, lakini ukienda Kenya utaona kabisa Kenya wameweka 16 percent VAT lakini huku sisi tumeweka 18 percent VAT na kodi mbalimbali zingine. Kwa kufanya hivyo wamefanya viwanda vingi viende vikaanzishwe Kenya na wamefanya sasa iwe kwamba kununua oil Kenya ni rahisi kuliko kununua oil hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Waziri, yeye pamoja na Waziri wa Fedha wakae chini waone namna ya kupunguza na kuondoa kodi hizi mbalimbali ambazo zitaweka usawa wa nchi za East Africa ili kuwawezesha wawekezaji kwenye maeneo haya kuja kuwekeza viwanda vikubwa vya kutengeneza oil hapa nchini, oil iliyo na ubora, oil ambayo yenye kiwango kilichothibitishwa na TBS ili kuondoa hili wimbi la kuingiza oil chafu kwenye maeneo ya nchi yetu hii.

Mheshimiwa Spika, mwisho kwa Mheshimiwa Waziri nataka nizungumze habari ya vijana wetu ambao wanasoma masuala ya umeme kwenye vyuo vyetu. Tunao vijana wengi wamesomea umeme, wamehitimu kwenye vyuo vyetu, lakini hii kwa mkakati alionao Mheshimiwa Waziri wa kupeleka umeme kwenye vijiji na vitongojini tunategemea mafundi ambao wanaenda kufanya installation kwenye nyumba za watu wetu kwenye maeneo yale leo hii hawajathibitishwa, hawajapata ithibati, hawajawa registered kwenye CRB. Matokeo yake ni kwamba mtu anakwenda kufunga umeme kwenye nyumba, anatumia kiasi cha shilingi 50,000 mpaka 100,000 kwenda kumuona mkandarasi tu amgongee muhuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Sasa nimuombe, ili kutengeneza ajira ya vijana wetu hawa ambao wamemaliza chuo kwenye maeneo hayo muweke utaratibu mzuri wa kuwasajili hao vijana ambao wamemaliza chuo waliyosomea mambo ya umeme, waweze kuwa na uwezo wa kwenda kuhakikisha ya kwamba wanathibisha na kugonga mihuri fomu zile kuondoa usumbufu na kutengeneza ajira kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo niombe sana, gharama, kama alivyosema hapa Mbunge mwenzangu Kenneth Nollo, muangalie na mtuambie ukweli gharama ya shilingi 27,000 inalipa? na kama hailipi mje na mkakati wa kuona namna gani mnaboresha. Kwa sababu utaona wametangaza shilingi 27,000…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimiwa kengle imeishagonga, malizia sentensi. (Makofi)

MHE. IDDI. KASSIM IDDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Wao wametangaza shilingi 27,000, lakini ukiangalia mtu unakwenda kuvuta umeme fundi anachaji 100,000 kwa ajili ya kugongewa muhuri, lakini pia kufanya installation kwenye nyumba ni zaidi ya 100,000 mpaka 200,000. Kwa hiyo gharama inarudi kule kule. Kwa hiyo niombe waliangalie suala hili haraka iwezekanavyo na watueleze ukweli wa jambo hili ili tuweze kuwaelewesha wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kusema hayo, ninaomba kuunga mkono hoja kwa asilimia 100. Nampongeza sana Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa unayo endelea kuifanya, ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. IDD K. IDD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuchangia Bajeti Kuu ya Serikali. Kwanza kabisa, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia leo kupata nafasi ya kuchangia bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Pia nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mwigulu Nchemba kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya pamoja na Naibu wake Waziri naye ameendelea kufanya kazi nzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nataka kujikita kwenye mambo machache sana. Moja, niendelee kuipongeza sana Serikali kwa bajeti hii ambayo imeileta hapa mezani. Ni bajeti nzuri, ni ambayo kama itaenda kutekelezeka kwa asilimia mia moja, basi italeta matunda makubwa sana kwenye maeneo yetu. Nimeona Wizara ya Nishati imeweza kuweka nguvu kubwa katika kuhakikisha kwamba inapeleka umeme kwenye maeneo yetu. Sasa niombe sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha aweze kutoa support kubwa sana kuhakikisha kwamba anapeleka fedha kuwalipa wakandarasi ili waweze sasa kuona namna gani wanaweza kuendelea na kazi ili ifanyike haraka sana ya kupeleka umeme kwenye maeneo ya vijiji vyetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ifanyike hivyo hivyo kwenye barabara na niombe sana Waziri wa Ujenzi, Jimbo la Msalala lina barabara moja ambayo tayari inafadhiliwa na Mgodi wa Barrick na niwapongeze sana Barrick kwa kuendelea kuonyesha jitihada za kuhakikisha kwamba wanatoa ushirikiano kwa Serikali ili kuona namna ya kujenga barabara hiyo. Niombe sana kwa Waziri wa Ujenzi, waone namna gani ambayo wanaweza wakapeleka mchakato huu haraka ili ikiwezekana basi mwezi unaokuja barabara hii ianze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hii imekuwa ni barabara ambayo ina kero kubwa sana. Watu wanapata ajali nyingi, magari yanadondoka na hasa magari yanayobeba mizigo mikubwa. Kwa hiyo, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na Waziri wa Ujenzi waweze kuharakisha mchakato huu ili barabara hii ianze kujengwa, kwa sababu fedha zipo kila kitu kipo tunasubiri tu mchakato ukamilike ili barabara ianze kujengwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo hivyo kwenye barabara zingine ambazo zimetajwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi, basi ni vyema pia Mheshimiwa Waziri baada ya hapo kwenye bajeti ya mwaka unaoanza akapeleka fedha mapema ili barabara hizi ziweze kujengwa, zirahisishe kujenga uchumi wa maeneo yetu hasa katika Jimbo la Msalala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie mambo mawili. Jambo la kwanza nataka nizungumzie habari ya oil ambayo imekuwa ni changamoto kubwa kwenye nchi yetu hii ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyofahamu Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kaka yangu January Makamba amekuwa akizungumzia sana habari ya mafuta na pia akaacha kuzungumzia habari ya oil ambayo pia inatumika katika maeneo mengi sana. Sisi tunatumia kwa ajili ya magari na vyombo vya moto vyote. Sasa kumekuwa na changamoto, nakubaliana kabisa na Mheshimiwa Waziri kwamba makubaliano ambayo huwa wanaaingia pamoja na Nchi za Afrika Mashariki katika kuweka ushuru wa malighafi ya oil kuingiza nchini kwa kiwango cha asilimia 10. Hata hivyo, niendelee kuomba sana, makubaliano ambayo huwa wanaingia huko kwenye Nchi za Afrika, wenzetu wanakuja kurekebisha kodi mbalimbali za ndani kuhakikisha kwamba wanajenga mazingira ya uwekezaji mzuri kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri kwenye suala zima la oil, aende akafanye mabadiliko, afute VAT na apunguze kodi mbalimbali zitakazowezesha wananchi kuingiza malighafi ya oil ili waweze kuwekeza viwanda vingi na tuweze kuzalisha oil hapa hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwani utaona kabisa kwamba kwa sasa hali ilivyo ni rahisi kununua oil katika nchi zingine, nchi za Jirani kwa sababu oil ni bei rahisi kuliko kununua oil hapa nchini hii. Hii inasababishwa na kuweka kodi mbalimbali kwenye malighafi ambayo inakuja hapa kwenye viwanda vyetu ambayo itazalisha oil hiyo. Kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, aende akakae, aangalie kama inawezekana wapunguze hiyo gharama ya kuingiza/kutoza malighafi ambazo zinakuja kuzalisha oil kwenye viwanda vyetu hivi vya ndani. Hii itasaidia kuhakikisha kwamba wananchi sasa wanaenda kuwekeza kwenye sekta ya kutengeneza oil.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nirudi kwenye suala zima la Jimboni ambalo wananchi wa Msalala wamenituma na hasa kwenye Sekta ya Madini. Mheshimiwa Waziri hapa naomba anisikilize vizuri sana, kuna jambo linaendelea la asilimia mbili kwa wachimbaji wadogo wadogo. Niombe sana, asilimia mbili hii nimehudhuria semina mbalimbali za watu wa Waziri wa TRA, wakitoa ufafanuzi juu ya asilimia mbili kwa wachimbaji. Mheshimiwa Waziri ameweka asilimia mbili kuanzia mchimbaji yeyote yule mwenye mapato ya kuanzia zero mpaka milioni mia ndiyo atayehusika na kulipa asilimia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimwambie Mheshimiwa Waziri, kama hataweka mfumo mzuri, wachimbaji wadogo wadogo mitaji yao inaanzia milioni mia na kuendelea juu. Sasa niombe kama tutaenda kupitisha hii asilimia mbili kwa wachimbaji wadogo wadogo, basi tuongeze kutoka kipato cha asilimia zero kwenda mpaka bilioni tano kwa sababu uchimbaji wa madini si kama biashara nyingine. Uchimbaji unaanzia kwenye mtaji mdogo sana, ni milioni mia moja kwenda juu. Kwa hiyo Waziri akisema kwamba mtu atakayechajiwa asilimia mbili ni kuanzia zero mpaka mia moja, maana analenga wale wachimbaji wadogo wadogo akinamama ambao wanaenda kuokota mifuko michache na kwenda kuchoma kupata gramu mbili, tatu kwa ajili ya kuendesha maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, hii asilimia mbili haiendi kumsaidia mchimbaji mdogo mdogo isipokuwa waje na mfumo, waweke utaratibu mzuri wa kwenda kuona ni namna gani wanaweza kuwajengea mfumo mzuri wachimbaji wadogo wadogo ili waweze kutunza hesabu zao na waweke mfumo mzuri kuona namna gani wanaweza kukubaliana na matumizi ambayo yanafanyika kwenye maeneo yale, kwa sababu kwenye maeneo ya wachimbaji wadogo wadogo ni nadra sana kumkuta mama ambaye anauza maji ana risiti, ni nadra sana kumkuta mtu ambaye anauza matimba ya kufunga mle ndani ana risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nashauri TRA na Mheshimiwa Waziri wa Fedha wakae na timu yake waangalie ni namna gani sasa wanaweza kuweka mfumo mzuri utakaomwezesha mchimbaji mdogo anapokuja kufunga hesabu zake kwa mwaka, baadhi ya matumizi wayakubali. Kwa hiyo wafanye research, waje na utaratibu huo, lakini wakisema kwamba mchimbaji mdogo mdogo alipe asilimia mbili, hii asilimia mbili haiendi kumgusa mchimbaji mdogo mdogo, isipokuwa inaenda kumgusa mama mnyonge kabisa ambaye anaenda kufanya sisi tunaita ukwale, mifuko miwili, mitatu, anaenda kusaga, anapata pointi mbili, gramu mbili ndiyo hii sheria ambayo wameileta ya asilimia mbili inaenda kum–favor, lakini kwa mchimbaji mwingine yeyote yule ile asilimia mbili haiendi kum–favor kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawataweka utaratibu wa namna gani wanaweza kukubaliana na matumizi ili mchimbaji huyu aweze kuweka gharama zake vizuri, itakuwa ni changamoto sana. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri, hii asilimia mbili ikiwezekana waende kuipitia upya, waiache kwanza, tukae vizuri kuona namna gani tunajadiliana, ni yupi atakayeweza kunufaika na hii asilimia mbili. Kama mapato yatakuwa ni asilimia zero mpaka bilioni tano tunakubaliana na hii asilimia mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ailete na sisi tutaipitisha, lakini kama ni mapato kuanzia asilimia zero mpaka milioni mia moja, biashara ya dhahabu siyo biashara ya vitumbua. Biashara ya dhahabu mtaji wake duara moja tu gharama yake ni milioni mia tano mpaka bilioni moja. Sasa Waziri akisema asilimia asilimia zero mpaka mia moja, maana yake bado ni changamoto na wachimbaji watakuwa hawajaelewa chochote kile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, nizungumzie habari ya leseni. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Madini, Mheshimiwa Doto Biteko, anafanya kazi kubwa sana. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, leo hii utaona wachimbaji walikuwa kupata leseni ni kazi sana, lakini ukisoma Ripoti ya Wizara ya Madini, utaona kabisa wamegawa leseni nyingi kwa wachimbaji. Leo hii tuna uhuru wa kumiliki leseni kwenye maeneo yetu, lakini bado kuna changamoto hapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika baadhi ya maeneo ya wachimbaji wadogo wadogo, kumekuwa na wawekezaji ambao wanatoka nje kuja kuchukua leseni hizi kubwa kwa maana ya prospecting license na leseni hizi hawaziendelezi. Wanapokuja kuchukua maeneo haya, wanatoka hapo baada ya kupatiwa leseni ya prospecting license wanaenda na documents zetu kwenda nje kutafuta mikopo na mikopo ile hairudi kuja kuendeleza leseni zile. Matokeo yake wanachukua zile fedha wanaenda kufanya mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe, kuna wachimbaji ambao tayari wapo kwenye maeneo yale, kwangu ukiangalia kuna maeneo ya Nyangalata, kuna maeneo ya Segese na maeneo mengine yote, kuna wachimba wengi ambao wanahitaji kuchimba na wamewekeza kwenye leseni zile za prospecting license, lakini bado hawajapatiwa leseni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri aje na mfumo kuhakikisha kwamba wale ambao wanapatiwa leseni za prospecting license hawazifanyii kazi, utaratibu ufanyike ikiwezekana kuwafuta ili wapewe wachimbaji wadogo wadogo waweze kufanya kazi, kwani wachimbaji wadogo wadogo kwa sasa ndiyo wanaochangia mapato makubwa kwenye Sekta hii ya Madini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri Biteko anapokuja ku-wind up hapa aje na kauli atueleze je, ni vipi sisi wachimbaji wadogo wadogo ambao tuko kwenye maeneo ambayo yameshikiliwa na leseni kubwa na leseni kubwa hizo hazifanyi kazi, namna gani anaenda kuzifuta ili wachimbaji wadogo wadogo tuweze kunufaika na maeneo hayo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia ripoti hizi tatu, Ripoti ya PAC, PIC, LAAC. Pia, nichukue fursa hii kwanza kabisa kumshukuru Mungu Azza wa Jalla kwa kunijalia siku ya leo kuamka salama na mimi kupata nguvu ya kuchangia ripoti hii ya leo. Pia, nimshukuru Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya.

Mheshimiwa Spika, anafanya kazi kubwa sana kuhakikisha ya kwamba anatutafutia fedha nyingi sana na kuzileta hapa nchini ili ziweze kutekeleza miradi mbalimbali. Ni ukweli usiopingika, mama yetu Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anapambana usiku na mchana kuhakikisha ya kwamba taifa letu la Tanzania linajenga mahusiano mazuri nje ya nchi lakini pia, linatengeneza fursa ya kupatiwa fedha mbalimbali zinazokuja hapa nchini ili ziweze kutekeleza miradi hii.

Mheshimiwa Spika, nilishuhudia siku moja nikiwa kwenye mkutano mmoja, siku ya walimu duniani. Mheshimiwa Rais alipiga simu akaongea hadharani kuwapongeza walimu siku yao ya walimu Tanzania.
Mheshimiwa Spika, baada ya hapo alisema yupo safarini anaelekea India na akasema ninaenda India wanangu kwenda kuwatafutia fedha. Ni ukweli usiopingika kwamba Mheshimiwa Rais amekuwa na kasumba ya kusafiri kwenda kutafuta fedha na fedha hizo zinakuja kwenye nchi yetu ya Tanzania. Kazi ya kusafiri kwenye ndege si kazi rahisi. Inawezekana watu wengine wakahisi kusafiri kwenye ndege ni furaha na starehe, kazi ya kusafiri na ndege ni kujitoa muhanga kwa sababu, wakati wowote ule likitokea la kutokea wewe safari yako imeishia hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kazi ya kusafiri kwenda kutafuta fedha si kazi rahisi. Hivyo, hatuna budi sisi kama Waheshimiwa Wabunge wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania kumsaidia kuhakikisha kwamba fedha ambazo anazileta hapa nchini zinaenda kufanya kazi iliyokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, sitaki kurudia, mambo mengi yamezungumzwa hapa. Amezungumza Mheshimiwa Luhaga Mpina juu ya Lot namba 3&4 ya reli, wamezungumza hapa habari ya TANOIL, wamezungumza hapa habari ya fedha ambazo zimepotea katika ukusanyaji wa mapato kwenye halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, mimi niseme, inawezekana chanzo cha upotevu wa fedha, chanzo cha mafisadi kwenye nchi hii ni kizazi ambacho sisi wenyewe tumekiandaa. Mimi ninapenda kuchukua fursa hii kuishauri Serikali. Moja, iweke utaratibu kabla ya vijana wetu na vijana wenzetu kupatiwa ajira, moja kuanzishwe chuo maalumu cha uwajibikaji ili kabla ya watu hawa kwenda kuajiriwa Serikalini wapite kwenye chuo cha uwajibikaji ambacho kitakachowafundisha namna bora ya kwenda kuwajibika kwenye taifa letu hili la Tanzania.

Mheshimiwa Spika, sambamba na kuwaelekeza wawe wazalendo kwa nchi yao hii ili waweze kutimiza majukumu yao ya kuwasaidia Watanzania. Ninaamini kabisa, kama mpango huu utaanzishwa unaweza ukarekebisha taifa hili la Tanzania kuwa na watumishi ambao wana maadili.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba, hapa tunapozunbgumza ninaona Mawaziri hapo wanachati. Mawaziri acheni kuchati, nisikilizeni hapa. Tusikilizeni. Mnanong’ona nini hapo? Lengo sisi hapa tunataka tuwasaidie nyinyi. Tunataka tumsaidie Mheshimiwa Rais fedha hizi zinazotafunwa za wananchi walipa kodi… (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Waheshimiwa Wabunge, Mheshimiwa Mbunge anachangia tujitahidi kusikilizana, tupunguze sauti tafadhali. Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Niseme tu Waheshimiwa Mawaziri mtuheshimu Wabunge, heshimuni Wabunge. Nyinyi mmekuwa tukiwapigia simu, amezungumza Mheshimiwa Maganga hapa, mimi nampinga kwamba Wabunge tunafanya nini?

Mheshimiwa Spika, Wabunge tunatekeleza majukumu yetu huko tunapoona ubadhirifu kwenye maeneo yetu huwa tunawatumia meseji na kuwaeleza Waheshimiwa Mawaziri juu ya mambo yanayoendelea kule lakini hawachukui hatua. Ninao ushahidi hapa kwenye meseji, sitaki kumtaja leo, nimemtumia Waziri kumweleza juu ya fedha ambazo Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameleta kwa ajili ya ujenzi wa shule na shule hiyo haijakamilika.

Mheshimiwa Spika, nimemtumia meseji kumweleza juu ya fedha za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ameleta kwa ajili ya kukamilisha zahanati hazijakamilisha na zimeibiwa fedha lakini hawajajibu na hakuna hatua zozote zile zinazochukuliwa, matokeo yake wanatuchonganisha Mawaziri na watumishi wetu kwenye maeneo yale. Tunapowaambia matatizo ya fedha kuibiwa kwenye maeneo yetu wanarudisha taarifa kwa watendaji wetu wa kule kututengenezea fitina sisi Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, hii haikubaliki, haikubaliki, mtaona ya kwamba labda tunawaonea wivu lakini hatuwaonei wivu, sisi tuko hapa kuwasaidia wananchi, tuko hapa kumsaidia Mheshimiwa Rais.

SPIKA: Mheshimiwa Kassim kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jerry Silaa.

TAARIFA

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa rafiki yangu na swaiba wangu Mheshimiwa Iddi Kassim kwamba hoja ya Mheshimiwa George Simbachawene ya jana iliyoungwa mkono leo na Mheshimiwa Maganga ya wajibu wa Waheshimiwa Wabunge kwenye halmashauri zetu ni hoja ya kisheria na kikanuni; kwamba sisi ni wajumbe wa kamati za fedha na uongozi kwenye halmashauri zetu. Kwa hiyo masuala ya usimamizi wa fedha kwenye halmashauri sisi tuna nguvu ya kikanuni ya kusimamia kwenye halmashauri zetu na hatupaswi kutuma meseji kwa Waziri bali kutimiza wajibu wetu kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, jambo analolizungumzia Mheshimiwa Waziri Silaa liliombewa mwongozo hapa na kiti hakijatoa bado mwongozo. Sasa, pamoja na sheria kusema hivyo kama huo ndio uelewa sisi kama Wabunge sina hakika kuna Mbunge atasimama hapa ambaye halmashauri yake haipo kwenye taarifa ya CAG, kwa sababu kama sote taarifa zetu mbaya ziko kwenye taarifa ya CAG na sisi ni sehemu ya hicho kilichotokea hatuna sababu ya kukaa hapa ndani tukawa tunajadili hii taarifa. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, natoa huu ufafanuzi kabla ya mwongozo ili tuelewe tunasimama wapi. Huwezi kuwa mwamuzi kwenye kesi inayokuhusu; na kama sisi Wabunge kila mmoja wetu anahusika kwenye halmashauri zetu ambao ndio uhalisia; kama kila mmoja wetu anahusika na ule ubadhirifu iliofanywa kule hatuna mamlaka sasa hivi ya kukaa hapa ndani kujadili hiyo taarifa. (Makofi)

Waheshimiwa Wabunge, maana yake tutafute chombo kingine cha kujadili jambo hili na kufanya maamuzi. Kwa hivyo kwenye hili kwa sababu mwongozo uliombwa na haujatolewa tusubiri Mwongozo wa Kiti haya ni maelezo ya awali. Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi malizia mchango wako. (Makofi/Vigelegele)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana, lakini pia rafiki yangu Jerry mimi na wewe tunaheshimiana sana. Tulipo hapa tupo kumsaidia Mheshimiwa Rais hatuko hapa kutetea majambazi, hatuko hapa kutetea wizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema kwamba kianzishwe chombo cha kufundisha uwajibikaji kabla ya watumishi kwenda kupata ajira mpya Serikalini. Ni ukweli usiopingika karne ya sasa mtumishi yeyote yule akiajiriwa leo anataka aanze kuishi maisha kama ya Mo Dewji, anataka aanze kuishi maisha kama ya GSM na watu wengine, matokeo yake yanapelekea ubadhirifu mkubwa kwenye maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, imetajwa hapa moja ya Halmashauri ya Ushetu ambayo ni miongoni mwa Halmashauri inayopatikana kwenye Wilaya ya Kahama. Mimi nimpongeze CAG kwa kazi kubwa anayoifanya pia na mimi leo niseme kwamba CAG naye tuone namna ya yeye kurekebisha kuanzia ngazi ya mkoa kwenda huko na wao wana changamoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi halmashauri yangu imetajwa kuwa ni halmashauri iliyopata hati safi lakini mpaka mwenyewe najishangaa wakati mwingine hii hati safi tumeipataje! Yaani mimi mwenyewe najishangaa. Kuna ubadhirifu mkubwa unafanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii utaona kuna fedha za miradi ya CSR iko kule inatafunwa, kuna fedha zinapelekwa kule hazikamilishi miradi. Tumesema kwamba fedha zinakuja ziende zikakamilishe miradi, tumepewa fedha za kujenga shule, shule hajakamilika mpaka leo, matokeo yake ni nini? Matokeo yake wanaanza kutafuta fedha (cash) kwenye mapato ya vyanzo vingine wanaenda kuziba mapengo kwenye fedha ambazo zimeletwa na Mheshimiwa Rais zikamilishe miradi. Miradi haiendelei, fedha ile ambayo ingeenda kutumika kujenga darasa lingine inatumika kuziba mwanya wa wizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu unafanya kazi kubwa mno. Mimi wakati mwingine huwa nakuonea huruma, unazungumza mpaka sauti inakwama, majambazi haya hayakomi. Nikuombe utembelee pia Wilaya ya Kahama uangalie uone ni nini, inawezekana Halmashauri ya Ushetu kupata hati chafu ni kwa sababu kipindi hicho Mkurugenzi hakuwepo, hawa pia huwa na wenyewe…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Spika, Taarifa

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi muda wako umekwisha.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi hii. Kwa niaba ya wananchi wa Msalala naomba nichangie hotuba ya bajeti hii ya Wizara ya Nishati.

Mheshimiwa Spika, moja kwa moja nianze kwa kumpongeza Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika Taifa letu hili la Tanzania. Nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitampongeza Mheshimiwa Waziri Kalemani kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika nchi hii ya Tanzania na Deputy wake kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Nitakuwa mchoyo wa fadhila bila kuwashukuru watumishi wote wa Wizara ya Nishati kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kuchangia katika maeneo matatu. Nianze kuchangia katika suala nzima la REA. Mheshimiwa Waziri nikuombe suala la REA hili katka Jimbo langu la Msalala na Mheshimiwa Mbunge mwenzangu leo yule wa Zanzibar ametutania hapa kwamba mradi wa REA katika Jimbo langu la Msalala Mheshimiwa Waziri bado na wewe mwenyewe ni shahidi. Pia sijui ni kwa nini Jimbo langu la Msalala na Mkoa mzima wa Shinyanga tumekuwa na bahati mbaya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mbunge mwenzangu hapa tuna vijiji 92 katika Jimbo la Msalala lakini vijiji 63 bado havijapatiwa umeme. Siyo hilo tu hata mradi wa umeme jazilishi kwa maana ya desentification katika baadhi ya maeneo bado haujasambaa kwa uhakika. Nimuombe Mheshimiwa Waziri baada ya Bunge hili tuweze kuambatana kwenda katika Jimbo la Msalala tuweze kuzindua miradi mbalimbali inayoendelea, lakini pia tufike katika maeneo yenye changamoto za umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu na maeneo mengine ya Mkoa wetu wa Shinyanga ukosekanaji wa umeme unapelekea kuhatarisha ndoa za kina mama. Akina mama wanajitahidi sana kupika wali na kuhakikisha umenyooka lakini unakuwa ni bokoboko kwa sababu wanatumia mbinu ya kutwanga badala ya mashine za kisasa za umeme ambazo zitachambua mchele vizuri na kuwapelekea kupika wali ambao utapelekea kudumisha mapenzi ndani ya ndoa. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri chondechonde fika Jimbo la Msalala tuone namna gani tunaenda kuanzisha umeme katika Kata za Jana, Mwalugulu, Mwakata na kata zingine zote zilizoko katika Jimbo la Msalala. Kwa kufanya hivi utanusuru ndoa za kina mama. Nikuombe baada hapa twende tukanusuru ndoa hizo za kina mama wa Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie changamoto ya umeme katika uwekezaji. Katika Jimbo la Msalala wengi wetu ni wawekezaji katika sekta ya madini, tunategemea umeme ili shughuli hizi za uchimbaji ziweze kufanikiwa. Waziri alitoa maelekezo kwamba katika Kata ya Lunguya, Kijiji cha Nyangarata maeneo yote yenye machimbo wapeleke umeme. Nashukuru Mheshimiwa Waziri tayari umeme unaelekea katika Kijiji cha Nyangarata, lakini bado Ntambarare umeme haujafika. Haya maelekezo unayatoa huku Mheshimiwa Waziri watendaji wako hebu jaribu kuyafatilia wanayapuuza, ulisema utakapotoka waanze kupeleka umeme mara moja katika Kijiji cha Ntambarare Segese katika Kata ya Segese. Mheshimiwa Waziri hebu tusaidie kwa sababu ukuaji wa sekta ya madini katika Jimbo langu la Msalala tunategemea nishati ya umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kumekuwa na changamoto ya gharama. Wawekezaji wengi wanalia kwa sababu ya changamoto ya gharama na gharama hiyo ni KVA charges kama penalty. Unapoenda kuwekeza hao wateja wakubwa kuna gharama ambayo huwa inatozwa kama penalty kwa wawekezaji hawa na gharama hiyo inapelekea kuleta changamoto kubwa katika uwekezaji. Leo hii mtu analipa gharama ya umeme mathalani shilingi milioni 40, lakini hapo anapigwa penalty kwa ajili ya matumizi ya umeme wa ziada ambao yeye hautumii. Niiombe Wizara hebu jaribuni kuona ni namna gani sasa mnaenda kutupunguzia charges hizi na ikiwezekana mziondoe ili ilete unafuu kwa wawekezaji wetu katika maeneo hayo ya migodi na viwanda vikubwa katika Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia ni namna gani mnaweza kuimarisha ugawaji wa transformer katika maeneo mbalimbali katika Jimbo langu la Msalala lakini pia katika maeneo mengi nchini kote. Nimekuletea concern za wafanyabiashara wengi ambao mpaka sasa viwanda vimesimama kwa sababu ya ukosefu wa transformer. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri bajeti hii itakapoenda kupita uone namna gani unaenda kuimarisha suala zima la usambazaji wa transformer kwa wafanyabishara wetu hawa katika maeneo yale ili na wao waweze kuendeleza viwanda vyao hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa nafasi hii, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa nafasi ya kuchangia. Pia namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan kwa kutuwakilisha vyema nje ya nchi na kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya kwa Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuipongeza Wizara ya Nishati na Madini kwa kazi kubwa wanayoendelea kuifanya. Nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Nishati na Mheshimiwa Waziri wa Madini, kwa kweli wanafanya kazi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niende kuchangia kwenye sekta ya madini. Tumeona, na ninawapongeza sana Wizara kwa kuhuisha Shirika letu la STAMICO. STAMICO wanafanya kazi kubwa sana. Ukilinganisha STAMICO ilipokuwa na sasa, unaona maendeleo makubwa sana; na tunaona uendelezaji wa ununuzi wa mitambo kwa ajili ya kusaidia wachimbaji wadogo wadogo umeshika kasi kubwa sana kwa sasa. Niendelee kuwaomba STAMICO pia waendelee kuondoka sasa kwenye maeneo ya uwekezaji mkubwa, waje sasa moja kwa moja kwenye uwekezaji wachimbaji wadogo wadogo katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona sekta ya madini wachimbaji wengi katika nchi hii hawana lesseni. Naomba Wizara, sisi tunaishi katika maeneo ambayo yana wachimbaji, maeneo mengi yamekamatwa na wachimbaji wenye PL na leseni kubwa. Leseni hizi ukiziangalia, bado watu hawazifanyii kazi. Kwa hiyo, naiomba Wizara kwamba wahakikishe wanaenda kuzipitia upya leseni hizi zote na ikiwezekana waweze kuzifuta wazirejeshe kwa wachimbaji wadogo wadogo ili wachimbaji wadogo wadogo waweze kupata leseni za uchimbaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sitarudia aliyosema Mheshimiwa Musukuma kwenye Nishati; sisi tunaotoka kwenye majimbo ya vijijini tumeona kata zetu nyingi na vijiji vyetu vingi bado havina umeme na mabadiliko ya bei yaliyotoka ya shilingi 27; katika maeneo yetu huko kwenye ngazi za mkoa kuna maelekezo yametoka ambapo yanataka maeneo ya vijijini ambapo kuna vituo vya afya, sekondari na shule, basi bei ile ya shilingi 27 inaenda kuondolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba kazi anayoifanya Mama Samia Suluhu Hassan katika maeneo yetu haya ni kuweka miundombinu ya vituo vya afya hasa vijijini. Sasa unapochukua kituo cha afya kama kigezo cha kubadilisha bei ya shilingi 27,000/= kwa wananchi wale, maana yake ni kwamba unaenda kuwaumiza wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri yuko hapa, naomba alichukue hili, aende akapitie upya maelekezo hayo, aondoe; kwa sababu vijiji vyetu ukiangalia, center zake zina umbali mrefu wa kilometa moja. Unapochukua kigezo cha pekee kuwa na kituo cha afya ndiyo kigezo cha kuchajiwa 320 siyo sawa. Wananchi wetu bado wanahitaji umeme. Namwomba Mheshimiwa Waziri afute kauli hii, wananchi wetu waweze kupata haki ya umeme katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niende kwenye suala nzima la barabara na sisi wanashinyanga hasa Mkoa wa Shinyanga tunahitaji huduma ya usafiri wa ndege. Tuna kiwanja chetu Mkoa wa Shinyanga, tumepata ufadhili kati ya Serikali na Benki ya European Investment Bank ya European Investment ambayo imetoa kiasi cha shilingi bilioni tatu na Serikali imetoa shilingi milioni 600 kwa ajili ya ujenzi wa kiwanja cha ndege Mkoa wa Shinyanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka ninavyozungumza hivi, Wizara imeshindwa kutoa shilingi milioni 500 tu kwa ajili ya kulipa fidia ili ujenzi uanze. Naomba Wizara, toeni fedha hii shilingi milioni 500 iende ikalipe fidia kwenye eneo lile ili uwanja wa ndege uanze kujengwa na wananchi wa Shinyanga nao wapate huduma ya ndege. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Leo ningependa kutoa mapendekezo yangu katika mpango huu wa Mwaka Mmoja wa 2023/2024 kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunafahamu kwamba Wizara na Serikali imetueleza hapa, kwamba imejipanga kuhakikisha kwamba inaboresha mazingira mazuri kwa wafanyabiashara hata hivyo pia mazingira mazuri katika ufanyaji biashara na uwekezaji katika nchi yetu hii ya Tanzania.

Leo mchango wangu na ushauri wangu utajielekeza kuielekeza Serikali kuongeza bajeti na kutenga bajeti na fedha katika kuhakikisha kwamba ina invest kwenye Jeshi letu la Polisi hasa katika kuwekekeza zana za kisasa katika kuweza kupunguza matumizi ya Askari Polisi barabarani. Ni ukweli usiopingika kwamba tunapozungumzia ukuaji wa uchumi na tunapozungumzia mazingira mazuri ya uwekezaji inaonesha ya kwamba ni lazima tutengeneze mazingira yanayoenda na uhalisia wa kumwezesha mfanyabiashara kutekeleza majumu yake kwa wakati au biashara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii utaona Jeshi letu la Polisi katika nchi yetu hii ya Tanzania imekuwa ni obstacle, imekuwa ni kikwazo kikubwa katika kuhakikisha ya kwamba inamwezesha mfanyabiashara kutimiza majukumu yake na kumwezesha kutimiza majukumu yake kwa wakati. Leo hii utaona unapozungumzia habari nzima ya uwekezaji ni lazima uzungumzie habari ya miundoimbinu. Serikali yetu nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa kuweka fedha kuimarisha miundombinu ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii utaona barabara ambayo Serikali ime- invest fedha nyingi ili kumwezesha mfanyabiashara huyu aweze kutimiza majukumu yake ya kwa wakati, Jeshi la Polisi na hususan Usalama wa Barabarani wanasimama barabarani kuhakikisha ya kwamba ukaguzi wa magari yale, pia mara zote kuhakikisha ya kwamba huyu mfanyabiashara anaweza kutoka hapa kwa namna moja ama nyingine wanaweza kumzuia mfanyabiashara huyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumejenga barabara ya njia Nane kutoka Dar-es-Salaam kuja mpaka Chalinze lakini utaona kila baada ya mita tano Askari Polisi hasa traffic hawa wamejaa barabarani, lengo ni ukaguzi ambao ukaguzi huu unamchelewesha mfanyabiashara kwenda kutimiza majukumu yake kwa wakati. Sasa niiombe Serikali iweze kuona namna gani inaweza ku- invest fedha ili iweze ku-invest kwenye Jeshi la Polisi kuwa na mitambo ya kisasa kuhakikisha kwamba inafanya kaguzi mbalimbali kwenye maeneo ya barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni suala zima la Madini. Niipongeze sana Wizara, mimpongeze Mheshimiwa Rais kuhakikisha kwamba anaweka jicho lake kumsaidia mchimbaji mdogo mdogo katika maeneo yale. Pia nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika sekta ya madini. Ninaomba na ninashauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha upo hapa, leo hii mchimbaji mdogomdogo hasa sekta ya madini na Mheshimiwa Rais alitoa maealekezo kwamba anahitaji Wizara ya Madini, iweze kuchangia Pato la Taifa sasa ili Wizara ya Madini, iweze kuchangia Pato la Taifa lazima Serikali iweke mkakati na bajeti kubwa kuhakikisha ya kwamba inamwezesha huyu mchimbaji mdogomdogo. Kwa hiyo, naomba nishauri Wizara na Serikali iweze kutenga fedha ili iweze kuwakopesha hawa wachimbaji wadogowadogo katika kwenda kufanya uwekezaji kwenye maeneo yao ili waweze kuzalisha kwa wingi na kuweza kuchangia Pato hili la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nizungumzie suala zima la barabara. Leo miundombinu ya barabara yetu katika maeneo yetu haya niipongeze Serikali na nimpongeze Mheshimiwa Rais kwenye Jimbo langu la Msalala, ametoa maelekezo kwa ajili ya ujenzi wa barabara yenye kiwango cha lami kutoka Bulyanhulu kwenda mpaka Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na urasimu katika utekelezaji wa miundombinu hii kwa wakati. Sasa niiombe Wizara kwamba ihakikishe pale ambapo tunatenga fedha na bajeti kwenda kujenga barabara wapitie upya mambo ambayo yanakwamisha utekelezaji wa miundombinu hii ya barabara ili kuwezesha barabara hizi ziweze kutekeleza kwa wakati na kumwezesha mfanyabiashara kutumia barabara hizi katika kutekeleza majukumu yake kiuchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara yangu ambayo tayari Mgodi wa Bulyanhulu umetenga fedha kiasi cha Dola Million 40 kwa ajili ya utekelezaji wa barabara. Barabara hii kwa muda mrefu sana tumeweza kuipambania Mheshimiwa Waziri wa Fedha ni shahidi, mpaka dakika ya mwisho Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan, ametoa tamko kwamba barabara ile sasa fedha ipo tayari na barabara ile ianze kujengwa maana ya kutoka Bulyanhulu mpaka Kahama, lakini leo hii utaona Wizara ya Miundombinu na Ujenzi kutoa tu kibali cha kuweza kuitangaza barabara hii ianze kujengwa mpaka leo bado hakijatoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe ili mpango huu ambao tunaujadili hapa uweze kutekelezeka kwa wakati ni lazima tupunguze urasimu ndani ya Serikali. Tunapanga mpango huu sisi wenyewe lakini sisi wenyewe hawa hawa tunaukwamisha huu mpango. Kwa hiyo, niombe sana Mheshimiwa Katibu mkuu wa Wizara ya Ujenzi, aweze kutekeleza maelekezo ya Mheshimiwa Rais ya kuanza kutangaza barabara hii na ianze kujengwa kwa wakati, barabara yenye kilometa 77 ambapo fedha zake anayelipa ni mgodi na mgodi upo tayari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inasikitisha sana leo hii tunaona fedha zile tumepewa na Mhisani hivi ikitokea leo madini yamepotea fedha zile tutazitoa wapi? Mlipaji yupo tayari na anataka kujenga barabara ile kwa wakati lakini Katibu Mkuu kutoa tu kibali barabara ile ianze kujengwa hajatoa mpaka leo ilkitokea leo madini yale yamepotea tunafanya nini? Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Madini
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwanza kabisa niende moja kwa moja kutokana na muda na nikuombe ikikupendeza basi unaweza kuniongeza dakika tatu ili niweze kuwasilisha hoja mahsusi.

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, pia nimpongeze Kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Doto Mashaka Biteko kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninakiri kwamba Mheshimiwa Waziri huyu anafanya kazi kubwa sana akisaidiwa na Naibu Waziri wake, na viongozi wote wa Tume pamoja na Wizara wanafanya kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nijikite kwenye ukurasa wa 32 ambapo Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake amezungumzia juu ya suala zima la CSR. Nitajikita kwenye suala zima la CSR lakini nitajikita kwenye suala zima la local content na nitajikita kwenye suala zima la fidia ambazo zinaendele kwenye maeneo ambayo tunatoka kwenye migodi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgodi wa Bulyanhulu ni mgodi unaopatikana katika Halmashauri ya Msalala, mgodi huu au maeneo haya ni maeneo ambayo yanachangia kiasi kikubwa kwenye Pato la Taifa hapa Tanzania. Mheshimiwa Waziri ametuambia hapa ni takribani zaidi ya Shilingi Bilioni 16 ambazo zimetolewa kama fedha ya CSR katika maeneo yetu na Msalala ikiwemo.

Mheshimiwa Spika, niseme tuna mgodi pale unaitwa Bulyankhulu, mgodi huu upo katika Jimbo langu la Msalala pia mgodi huu upo katika Jimbo la Mheshimiwa Waitara. ninakiri kwamba mgodi huu umeendelea kutumia fedha vibaya za CSR ambazo Mheshimiwa Waziri amezitaja hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Halmashauri ya Geita wanapokea kiasi cha Shilingi Bilioni 10 kama fedha ya CSR lakini Bulyankhulu na North Mara, Bulyankhulu tunapokea Bilioni 2.5 tu fedha ya CSR. Leo Mheshimiwa Waziri amezungumzia hapa kwamba fedha hizi zimeenda kujenga barabara, zimeenda kusambaza maji, zimeenda kujenga miundombinu ya elimu. Nikuhakikishie katika Jimbo langu la Msalala ambapo makinikia mengi yanachimbwa barabara hakuna.

Mheshimiwa Spika, utaona malori na Malori ya makinikia yakisafirishwa, vumbi kali wananchi wanapata taabu lakini hakuna tunachonufaika juu ya uwepo wa barabara. (Makofi)

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, kama ni taarifa nilinde utaniongezea dakika.

SPIKA: Muda hauongezeki nadhani tulishaambiana humu ndani, muda wa taarifa ni wewe unaongezewa kwenye mchango wako Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, ni kwamba nataka kumwambia mchangiaji kwamba katika hiyo CSR ya mgodi huo wa Barrick walitakiwa watengeneze barabara ya lami inaanzia hapo Kakola inakuja mpaka Busisi hawajatekeleza hilo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2000 na 2003 mgodi ya Bulyankhulu uli-declare kwamba ulitumia kaisi cha Shilingi Bilioni 50 kwenye miradi ya maendeleo kwenye maeneo yale, walitumia fedha zilezile za CSR kujenga nyumba za watumishi Bugarama na Ilogi.

Mheshimiwa Spika, TRA waliwasamehe kodi…

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge muda wenyewe wa kuchangia ni mfupi sana kwa Mbunge sasa taarifa zikiwa nyingi yeye mwenyewe atakuwa hamalizi, Mheshimiwa Waitara.

T A A R I F A

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba kule Nyam ongo waliahidi kujenga Chuo cha VETA chenye hadhi ya Wilaya tangu mwaka 1995, hawajajenga mpaka leo. (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, unaipokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa hiyo nikuombe uniongezee dakika tano. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Spika, walitumia fedha za CSR kujenga nyumba za wafanyakazi na waka-declare fedha zile kwamba wametumia kwenye kujenga miradi ya maendeleo, lakini cha kushangaza nyumba zile walianza kuuziwa tena watumishi na zile fedha hatujui mpaka leo zimeenda wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mgodi huo wa Bulyankhulu umekuwa ukilalamikiwa kila kona na tukisema hapa tunaambiwa jambo moja tu, kwamba mkisema mwekezaji huyu mkubwa tutakuwa blacklisted. (Kicheko/ Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa tunasema wananchi wa Jimbo la Msalala hasa Bulyankhulu, hatuko tayari kupata manyanyaso haya yanayoendelea kwa hofu ya kwamba tutafungiwa. (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana. Mheshimiwa Mbunge lakini nafikiri hoja yako imeeleweka na Mheshimiwa Waziri ni muhimu, nafahamu sheria inaweka mwongozo lakini ni muhimu ninyi kama Wizara kufuatilia hizi fedha zinazotolewa zinafanya kazi gani, kwa sababu bila kuwa mnafahamu zinafanya kazi gani ndiyo hivyo mtu anaamua kupeleka kule anakotaka yeye na siko kule wananchi wanakotaka fedha zipelekwe. (Makofi)

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipatia fursa hii ya kuchangia kwenye Hotuba ya Wizara ya Mambo ya Ndani.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya pia Naibu wake kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya lakini yote kwa yote nimpongeze sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya ya kuhakikisha ya kwamba Tanzania tunaishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo ninachangia mambo machache sana, nianze tu kwa kusema Jeshi letu la Polisi linafanya kazi kubwa sana. Nijikite kwenye kuzungumzia watumishi, Askari wetu waliopo kwenye maeneo yetu tunayotoka katika maeneo ya vijijini. Maeneo ya vijijini Askari wetu wanaishi katika mazingira magumu sana, pia ukiangalia Mishahara yao, ukiangalia kazi zao ni kwamba Jeshi letu la Polisi katika maeneo hayo ninayoyataja mara nyingi sana yanaendeshwa na wadau. Sasa hili limekuwa ni tatizo kubwa sana juu ya utekelezaji wa majukumu yao kama Askari, weledi kwa sababu mambo mengi yanaendeshwa kwa sababu ya wadau kutokana na changamoto ya kibajeti.

Mheshimiwa Spika, nimuombe sana Mheshimiwa Waziri ili kutunza heshima ya Jeshi letu hasa Askari wetu hawa, tuone namna gani sasa Serikali inaweza ikatenga fedha nyingi na kupeleka katika maeneo yale ili Askari wetu waweze kufanya kazi kwa weledi. Wanapotaka mafuta ni kwamba wanatafuta wadau, kila kitu ni wadau, Mheshimiwa Waziri kuna changamoto imeanza kuna mfumo umeanza wa kutoa hizi loss report. Hizi loss report Mheshimiwa Waziri kwa sasa utaona kabisa kwamba IGP amekaimisha mamlaka kwa OCS na OCS ameteua mtu kwa ajili ya ku-verify zile ripoti. Hasa ripoti hizi Mheshimiwa Waziri utaona kwamba huyu Askari aliyeteuliwa na OCS hajatengewa fungu la bundle, kuweka bundle ili aweze kuingia kwenye mtandao ku-verify zile loss repot. Maana yake ni nini tunawatengenezea mazingira ya Askari wetu hawa kwenda kuanza kutafuta wadau na kushusha heshima ya Jeshi. Niwaombe sana kuhakikisha ya kwamba wanatenga fungu la bundle, huyu mtu aliyeteuliwa ku-verify kwenye mfumo atengewe fedha asitegemee wadau.

Mheshimiwa Spika, pia nikazie kwa kusema kwamba Askari wetu hawa kuna suala zima la posho ya safari imekuwa ni changamoto Mheshimiwa Waziri. Tuhakikishe ya kwamba sasa Askari wetu hawa wanapotaka kwenda safari wanafanya kazi, tunatambua kazi ngumu wanazofanya huku, wanaposafiri sasa likizo maana yake ni kwamba wanategemea ile fedha watakayolipwa kwenye likizo lakini pia na posho ya safari iweze kuwasaidia katika ku-refresh mind zao kutokana kazi kubwa walizofanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii utaona kabisa kwamba hata fedha zao za likizo zimegeuzwa kuingizwa kwenye mfumo wa madeni tena. Kwa hiyo tunaendelea kuwanyonya bila kutambua Askari wetu hawa wanafanya kazi kubwa sana. Nikuombe Mheshimiwa Waziri haya nenda ukayashughulikie kuhakikisha Askari wanalipwa posho zao za safari kwa wakati, likini pia moja kwa moja fedha za likizo zisiende kuingizwa kwenye mfumo wa madeni wapewe fedha zao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende kusema kwamba tuna changamoto kwenye Jimbo la Msalala la ukosefu wa Kituo cha Polisi, hapa nikwambie Mheshimiwa Waziri ninaenda kukamata Shilingi ya Mshahara wako Mheshimiwa Waziri kama hautanipa majibu sahihi ya kwamba ni lini sasa Jimbo la Msalala tunaenda kuwa na Kituo cha Polisi.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kahama ina Majimbo matatu, Ushetu, Kahama na Msalala lakini utaona kwamba tuna Ma-OCD kote kule, lakini hakuna vituo vya Polisi, hapo hapo vitendea kazi magari hakuna na nimeona Mheshimiwa Waziri umesema kuna ununuzi wa magari. Niombe kwetu kule OCD anatembea na boda boda lakini mbaya zaidi ni kwamba tuna mgodi katika maeneo yale lakini pia hata gari anayotumia aliyopewa ni ngumu kwenda kuhakikisha kwamba wanafanya patrol katika maeneo yale. Tuna Leyland moja imeletwa, kule kwetu Leyland huwa inatumika kubeba matimba kwenda machimboni. Sasa hii Leyland inatumika kufanya operesheni katika maeneo ya porini, nikuombe Mheshimiwa Waziri mnapoenda kutoa magari toeni magari kuzingatia maeneo husika ya mazingira halisi ya maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Leyland haiwezi ikapita kwenye barabara zetu kule kwenda kufanya operesheni. Mheshimiwa Waziri kwenye magari yale naomba Jimbo letu la Msalala liwe namba moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala jingine la NIDA. NIDA kumekuwa na changamoto kubwa sana na nimuombe Mheshimiwa Waziri akisimama hapa na nitashika Shilingi ya Mshahara wake, atueleze ni kwa nini hili suala zima la NIDA limechukua muda mrefu. Leo hili mwananchi wetu kila jambo analotaka kulifanya ni NIDA, anapotaka kwenda kusajili line NIDA, anapotaka kwenda kufanya jambo lolote inahitajika kadi ya NIDA na kama wameshindwa hivi leo hii kweli Serikali watu wa Uhamiaji tunazidiwa na Club ya Yanga, Club ya Yanga inagawa kadi. Kama wameshindwa waje walau wajifunze kwenye Club ya Yanga kuona ni namna gani hawa Club ya Yanga wanafanya kuhakikisha wanawapatia kadi wanachama wao. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niendelee kumuomba Mheshimiwa Waziri ninakuomba baada ya hotuba yako Mheshimiwa Waziri…

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi kuna taarifa ikitokea kwa Mheshimiwa Nicholaus Ngassa.

T A A R I F A

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Naomba nimpatie taarifa mchangiaji kwamba kadi zinazotengenezwa na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa za NIDA zile zinaitwa smart card maana yake zinazosomana na mifumo. Kwa hiyo, ndiyo maana unaona inaweza ikatumika kadi ya NIDA kusoma mfumo kwenye PSSF, NSSF au kwenye leseni tofauti na kadi zinazotolewa na wananchi - Yanga ni kadi ambazo haziwezi kusomana popote kwenye mfumo.

Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa. (Makofi/Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, umepokea taarifa hiyo?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, taarifa ya Mheshimiwa Ngassa siipokei. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, niendelee kuwaomba, niendelee kuwaomba hivyo hivyo Chama chetu cha Mapinduzi kinatoa kadi hizi ambazo zinaendana na mfumo anaousema huyo. Pia niwaombe waje wajifunze kwenye Chama cha Mapinduzi kuona ni namna gani tunatoa kadi zile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie suala zima la Magereza. Wilaya ya Kahama ina Gereza moja na Gereza lile ni dogo sana, nimeenda kufanya ziara mle na nilimwambia Waziri kwamba kuna changamoto ya ukosefu wa majengo.

Mheshimiwa Spika, ahsante. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwanza kabisa nianze kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu mpendwa, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya. Pia nampongeza Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu wake na Watumishi wote wa Wizara ya Mifugo. Nami leo nimewiwa kuchangia kwenye bajeti hii ya mifugo na ninataka nimwambie tu Mheshimiwa Waziri kwamba, kwenye Wilaya ya Kahama, Halmashauri ya Msalala, Jimbo la Msalala ni wafugaji wazuri sana wa ng’ombe. Nami nijikite sana kwenye kuzungumzia leo ufugaji wa ng’ombe kwa sababu ndiyo mifugo ambayo tunaifuga katika Jimbo langu la Msalala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Msalala, utaona kabisa wananchi wangu wanafuga ng’ombe kwa wingi. Changamoto kubwa iliyopo kwenye maeneo yale ni malisho pale ambapo mifugo inaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna minada mingi ya ng’ombe kwenye maeneo yale. Tuna wafugaji wengi kwenye maeneo yale. Nampongeza sana Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan, kupitia Mheshimiwa Waziri wake kwa kuweza kutupatia ng’ombe madume 50 ya ng’ombe ambayo kimsingi yanaenda kuzalisha ng’ombe wa kutosha kwenye eneo lile la Jimbo langu la Msalala. Hawa ng’ombe 560 hawataweza kusaidia, na kwa sababu ni ng’ombe wa kisasa hawataenda kuwasaidia wananchi wangu kama hatutatenga bajeti nzuri ya kuweza kwenda kujenga miundombinu rafiki kwenye mifugo hii ambayo tayari tumeshaipeleka kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati tunapokea ng’ombe hawa, maelekezo tuliyopewa ni kwamba, ngombe hawa wanahitaji kuoga mara kwa mara; ng’ombe hawa ni adui wakubwa wa kupe. Sasa kwenye maeneo yetu, hasa kwenye Jimbo la Msalala, utaona miundombinu ya majosho bado iko chini sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka jana wa fedha 2021/2022 tulipokea ahadi ya kupewa majosho matano, lakini ni majosho mawili tu yaliyokuja yakakarabatiwa na yale majosho matatu mengine bado hatujayapokea. Namwomba Mheshimiwa Waziri, kama tunataka kuilinda mifugo hii ambayo ninyi wenyewe mmetuambia ni delicate sana, inahitaji kuoshwa mara kwa mara, ni adui wa kupe, basi tuhakikishe kwamba kwenye bajeti hii mtutengee majosho ya kutosha ili mifugo hii iweze kuoga, na iwezeshe sasa wananchi kuitumia vizuri na kuzalisha ng’ombe wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali hapo nyuma ilizuia juu ya ugawaji wa ranch. Nami nikiri tu kwamba, kwenye maeneo yangu ukiangalia, wafugaji wengi wamekua kwa sasa. Kuna baadhi ya wafugaji wana ng’ombe kuanzia 500 mpaka 600, na hivyo kuwafanya waanze kuhamahama kwenye mapori. Wanapoenda kwenye mapori kule, matokeo yake wale ng’ombe wanakamatwa. Sasa naomwomba sana Mheshimiwa Waziri na Katibu Mkuu wake, hebu wachukue hili, waende wakaangalie lile zoezi la kupitia zile ranch ambalo walilisimamisha kufanya uhakiki halijakamilika? Kama limekamilika, hebu mwagawie sasa wananchi wetu kule ili waweze kufuga mifugo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hili aliandike kwamba wananchi wanahangaika kule, waende wakapitie haraka. Mkurugenzi huyu aende akafanye kazi haraka iwezekanavyo, watangaze ranch hizo wawagawie wananchi. Wanapata taabu kwenye maeneo yetu huku. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hapa kuna Mheshimiwa Mbunge mwenzangu wa Ushetu, kuna mwananchi wake alikuwa na ng’ombe zaidi ya 600, ng’ombe wale waliingia kwenye hifadhi na walikamatwa na uzuri alishinda kesi, lakini mpaka sasa bado hajalipwa fedha zake. Hii yote ni kwa sababu hatuna maeneo ya kuchungia mifugo yetu. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri awe mlezi kweli kweli.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa, Mheshimiwa Waziri, tunazungumzia habari ya wafugaji; yeye anasimamia wafugaji, lakini inapokuja kwamba mfugaji anapata changamoto, wanajitoa. Sasa naomba, hebu endeleeni kusimama na wafugaji. Mfugaji anapopata changamoto yoyote, mshikeni nendeninaye moja kwa moja kuhakikisha kwamba anatendewa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Mheshimiwa Waziri amekuja kutembelea kwenye Jimbo langu la Msalala, wakati anatukabidhi madume 50, sambamba na hilo aliahidi kutujengea bwawa la Mkoloni, Busangi. Ninaamini ahadi ile ilitolewa na Mheshimiwa Waziri ambaye alikuwa ni Mheshimiwa Mashimba Ndaki, yuko hapa; lakini Mheshimiwa Mashimba Ndaki hakutoa ahadi, aliyetoa ni Waziri, nawe umekaa hapo Mheshimiwa Waziri. Nikuombe chukua kalamu na karatasi Mheshimiwa Waziri, ahadi hii itekelezwe. Wananchi hawa tumewaahidi bwawa la kunyweshea mifugo kwenye Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kwamba tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi kwenye maeneo yale. Sasa namwomba Mheshimiwa Waziri aone katika bajeti hii, atuletee watumishi wengi kwenye sekta hii ya mifugo ili waende wakawasaidie wananchi kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa la mwisho, naomba nichangie kwenye suala zima la minada. Kwenye Jimbo la Msalala tuna minada takribani zaidi ya 10, na minada hii inafanya kazi vizuri sana. Kwenye Wilaya ya Kahama Halmashauri pekee yenye mifugo mingi na yenye minada mingi ni Halmashauri ya Msalala. Sasa changamoto inakuja, hawa watu wanapoenda kuuza mifugo yao, Halmashauri inawa-charge fedha. Kwa mfano, kwenye ng’ombe wanachajiwa shilingi 7,000 kwa ng’ombe, lakini shilingi 3,500 inakatwa moja kwa moja kwenda kwenye Serikali Kuu na haiingii hata kwenu kwenye Wizara, inaenda moja kwa moja kwenye Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimwomba Waziri wa Fedha, yuko hapo, fedha ile inapokatwa muweze kuwa mnarudisha percent kwa ajili ya kwenda kufanya ukarabati wa miundombinu. Ukienda kwenye minada hii, unakuta choo hakuna, miundombinu ni mibovu, lakini wananchi wanalipa fedha. Pia Halmashauri zimeanza kuogopa kufanya uwekezaji wa kuendeleza minada hii kwa sababu fedha hawapati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unakuta Halmashauri imewekeza zaidi ya Shilingi milioni 200 kukarabati mnada, lakini hapo hapo ninyi mkiona mnada huu umependeza, mnauchukua tena moja kwa moja na fedha zote Halmashauri haipati, zinaenda Wizarani. Sasa naomba, kama Halmashauri inaenda kuwekeza fedha kwenye minada yake, hebu mtuachie tuweze kuiendesha minada hiyo, nanyi msiingilie, mtuachie wenyewe Halmashauri, ili Halmashauri ziwe na moyo wa kuendelea kuwekeza kwenye maeneo hayo. Pia fedha hii ambayo inakatwa kwenda Serikali Kuu, hasa kwenda kwenye Wizara ya Fedha, fedha ile basi iweze kukatwa asilimia kadhaa, ije irekebishe maeneo ya miundombinu kwenye maeneo yale, hasa vyoo na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo, nakushukuru sana, lakini ahadi hii ya majosho matano mpaka leo hatujui yako wapi, iandike. Ahadi ya Bwawa la Mkoloni, Busangi ni muhimu sana kwa sababu ni ahadi ya kiongozi ambaye aliitoa, ni Waziri, nawe uko hapo umekalia kiti hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa fursa hii ya kuweza kuchangia mchana wa leo katika Hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Kwanza kabisa nampongeza Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, pia kwa jitihada kubwa ambazo Mheshimiwa Waziri amezizungumzia hapa; kutafuta fedha mbalimbali katika kuhakikisha kwamba wanaboresha mifumo kwenye Jeshi letu hili la Polisi na majeshi mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwa kazi kubwa unayoendelea kuifanya. Mimi kama mdogo wako, nina imani kubwa sana na wewe na uwezo wako ulionao. Wewe pamoja na Naibu Waziri wako. Nataka nikusihi jambo moja tu Mheshimiwa Waziri kwamba utaandika kitabu chenye historia nzuri sana kama utafanya mabadiliko na mapinduzi makubwa sana katika kuliboresha Jeshi la Polisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jeshi la Polisi kwa sasa ukienda kwenye mawanda ya ajira utaona kabisa imepewa kipaumbele cha mwisho katika kutafuta ajira ama kuombwa ajira. Uki-compare na hapo mwanzoni Jeshi la Polisi lilivyokuwa lilikuwa na heshima kubwa sana. Leo hii tuna baadhi ya Maafisa wa Polisi wakubwa tu akiwemo IGP mwenyewe Wambura, wakiwemo akina Msangi, akina Mkumbo nimemwona hapo na wengine, akiwemo RPC wangu wa Shinyanga Mama yangu, ni mfano ulio bora kwa maafisa wenye weledi, wanafanya kazi vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kadiri siku zinavyokwenda Mheshimiwa Waziri mwenyewe umeona kumekuwa na sintofahamu ndani ya Jeshi la Polisi. Nidhamu, weledi, rushwa na mambo mengine. Haya yote kama alivyosema kaka yangu Mheshimiwa Shabiby hapo, ni kwa sababu maslahi ya Askari wetu ni mabaya mno. Askari ambao wanatulindia mali zetu, Askari ambao wana-risk maisha yao, leo hii Askari anayefanya kazi miaka 60, anapostaafu, anaondoka na Shilingi milioni 18. Hivi hata kama ni wewe Mheshimiwa Waziri, usingefurahi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado hata pension utaona, mtu aliyetumikia Taifa kwa miaka zaidi ya 60 anaondoka na Shilingi 40,000. Ndiyo maana nikatanguliza kukuomba kaka yangu, utaandika kitabu kizuri sana kama utaenda kusimamia vizuri kwa weledi maslahi ya hawa watu ili waweze kufanya kazi kwa bidii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kwenye Jimbo langu la Msalala. Wilaya ya Kahama ina Halmashauri tatu, lakini Halmashauri hizi kwa maana ya Ushetu, Msalala na Kahama Manispaa; Msalala tuna OCD, lakini OCD yule hana gari, OCD mwenyewe anakwenda kukagua tukio kwa bodaboda, akishuka pale amejaa vumbi, hata haeleweki. Nakuomba kaka yangu kwa uchungu mkubwa, maeneo yetu hasa sisi tunaotoka kwenye mazingira ya mgodi, cha kushangaza, hawa hawa ndio Askari ambao wanaenda kulinda mali, migodi mikubwa hii. Hivi Mheshimiwa Waziri unashindwa kufanya kikao hata na hawa wawekezaji wakubwa kwenye maeneo yetu kama Barrick kuwaomba walau wachangie magari kwa ajili ya maaskari wetu ambao wanalinda mali zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia askari hawa wamekuwa wakidharaulika kwenye maeneo mengine. Leo hii wanaacha kufanya kazi ya uaskari, kwenye maeneo yetu utakuta askari ndiyo mchimbaji anaingia kwenye duara. Kwa nini? Kwa sababu maisha ni magumu, hajielewi. Boresha maslahi Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunazungumzia habari ya rushwa. Rushwa inatokea kwa sababu ya mazingira magumu. Nenda kaimarishe mifumo kwenye Jeshi la Polisi. Siyo kila kitu kinaweza kikafanywa na watu wenyewe. Leo tunazungumzia habari ya tochi. Kwani hakuna mfumo, hakuna system ambayo unaweza ukaifunga Mheshimiwa Waziri? Cameras au kukawa na checking point walau kutoka hapa kwenda Dar es Salaam kukawa na checking point mbili? Funga camera, funga vifaa vya kisasa ambavyo vitasaidia kuonesha kwamba vinaweza kulinda usalama wa barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nizungumzie habari ya magari. Naomba sana, kwenye Jimbo la Msalala, Halmashauri ya Msalala, Halmashauri ya Ushetu, tusaidie magari. Bado mpaka sasa utaona, hata kwenye misafara hii, magari yaliyoletwa yale ya Land Cruiser wanazotumia ma-OCD, ma-RTO bado zimechoka mno. Unakuta Land Cruiser iko kwenye msafara, tairi inatembea inacheza inakatika, inakatika, inakatika. Naomba sana Mheshimiwa Waziri katika bajeti hii, pia peleka maombi kwa Mheshimiwa Rais aone namna ya kuweza kusaidia kununua magari mapya kwa ma-OCD wetu kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nizungumze habari ya vituo vya Polisi. Nampongeza sana RPC wangu wa Mkoa wa Shinyanga. Huyu mama anafanya kazi kubwa sana. Nimekuwa nikilia hapa toka mwaka 2022 kupatiwa vituo vya Polisi maeneo yetu hayo ni maeneo hatarishi sana maeneo ya migodi. Mama ameweza kufanya jitihada nami mwenyewe nimemchangia, sasa hivi tunanyanyua vituo vitatu vya Polisi Isaka, kituo kimoja kinanyanyuka na bado hakijakamilika. Naomba kwenye bajeti hii upeleke fedha tukamalize Kituo cha Polisi cha Isaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunanyanyua kituo kingine cha Polisi Kata ya Ngaya, tumeezeka, tunatakiwa tumalizie. Naomba muunge mkono RPC wako wa Shinyanga tukamalizie Kituo cha Polisi hiki. Tunajenga Kituo cha Polisi kingine Kata ya Mwaluguru kitahudumia kata tatu. Tayari kiko kwenye lenta. Nakuomba peleka fedha twende tukamalizie vituo hivi. Huyu mama ameona aanze jitihada mwenyewe binafsi kuhakikisha ya kwamba tunakuwa na vituo vya Polisi kwenye maeneo yale ili tuweze kulinda usalama wa raia na mali zao kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo, namwomba sana Mheshimiwa Waziri, hali ya vituo vya Polisi kwenye maeneo baadhi, ni mbaya mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukienda Kata ya Busangi tuna kituo cha Polisi lakini kimebomoka upande. Askari wamekaa mle ndani kwenye gofu. Muda wowote linaweza likadondoka. Kwa hiyo, nikuombe sana Mheshimiwa Waziri uone namna ya kupeleka upeleke fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho nizungumzie habari ya NIDA.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie hili la mwisho. Suala la NIDA, bajeti iliyopita ya mwaka 2022 nilizungumza hapa, nikasema suala la NIDA ni changamoto kubwa mno na nikatoa mfano nikasema mnazidiwa hata na Klabu ya Yanga! Leo hii kwenye maeneo yetu hakuna jambo lolote linaloweza likafanyika mpaka mtu awe na kadi ya NIDA. Mmefeli wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri wewe ni rafiki yangu, ni kaka yangu, lakini kwenye hili mimi nashika shilingi. Mheshimiwa Shangazi uko hapo, uniandike. Nashika shilingi ya mshahara wako mpaka uje unieleze, mna mkakati gani wa kuhakikisha ya kwamba mnatatua tatizo la kadi za NIDA?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kunipa fursa ya kuchangia leo katika bajeti ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kumpongeza Rais wetu mpendwa Mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya, kuipa uzito suala zima la michezo. Wote tutakuwa mashahidi baada ya kuona kazi kubwa inayofanyika na hasa kwenye sekta ya michezo, Mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu mpendwa amewekeza ametoa support kubwa kumaanisha kwamba sekta ya michezo imeshika hatamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimpongeze sana Rais kwa uzalendo wa kutoa fedha lakini pia kutoa ndege kuisafirisha Timu ya Yanga kwenda kushiriki mashindano ya shirikisho. Na hivyo nitumie fursa hii kuwapongeza sana Wananchi kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kuliletea heshima Taifa letu hili. Yanga wamefanya kazi kubwa sana ya kutuheshimisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme, na niwe mkweli hapa, kuna watu wanausemasema ushindi wa Yanga; naomba nikwambie kwamba ushindi Yanga tulivyoshinda ni tofauti na ushindi huo wanaouzungumzia enzi za Ukoloni, utaona kabisa Yanga tumeshinda aggregate, maana yake tumeshindwa kikanuni tu. Kwa hiyo niwapongeze sana wachezaji wote wa Timu ya Yanga, lakini niupongeze uongozi mzima na mashabiki wote wa Yanga, kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo mimi nataka nijikite hasa kwenye suala zima la sanaa na michezo kwenye Halmashauri zetu hizi za Msalala, Ushetu, Kahama na nyingine. Kwa suala zima la sanaa sisi tunaotoka kwenye maeneo megine, na hili nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, mama yangu, utakapokuja kusimama hapa, mtueleze, hivi hili suala la sanaa, michezo, wasanii kwa maana ya Bongo Fleva, waigizaji; hivi ni Dar es Salaam tu, maeneo mengine hatutambuliki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote ni mashahidi hapa, mtaona, wasanii wetu kwenye maeneo yetu wana vipaji vikubwa mno lakini hawana support. Lakini leo hii utaona vipaji vyote vinatoka Dar es Salaam, yaani ili mtu aweze kutoka kuwa msanii bora, ni lazima aende Dar es Salaam. Sasa wale wanaotoka kwenye maeneo yetu ni lini hasa watakuwa; ni lini hasa Serikali itatengeneza utaratibu mzuri, mfumo mzuri wa kuhakikisha kwamba na wale wanaotoka kwenye maeneo ya vijijini waweze kukua?

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Iddi Kassim, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Hamisi Taletale.

TAARIFA

MHE. HAMISI S. TALETALE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nimpe taarifa babu yangu, Mheshimiwa Sheikh Iddi Kassim, kwamba hawa wasanii ambao tunawaona Dar es Salaam siyo kana kwamba wanasaidiwa na Wana-Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano msanii kama Diamond anatokea Morogoro na Kigoma, amejisaidia mwenyewe kufika pale. Tusiupe mzigo Serikali kwamba watu wanaobakia Morogoro wasaidiwe na watu wa Morogoro. Kwa hiyo taarifa yangu ni kwamba, ndugu yangu, Mheshimiwa Iddi, kama unataka kuhamia Morogoro ili utoke karibu Morogoro, mlezi wa vipaji ni mimi hapa.

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Iddi Kassim, taarifa unaipokea?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo mimi siipokei kabisa kwa sababu ninao akina Babu Tale zaidi ya 20. Narudia; ninao akina Babu Tale zaidi ya 20 wako Kata ya Bulyanhulu, wana uwezo wa kusimamia wasanii kwenye maeneo yale. Tunao wasanii bora kwenye maeneo yetu, hasa Kata ya Bulyanhulu na maeneo mengine Kahama, tunao. Tunao waandaaji tuzo, wapo wengi, Mheshimiwa Naibu Waziri anafahamu. Sasa msitufanye sisi tunaotoka kwenye mikoa huko kuwa ni maeneo tu ya Mawaziri kuja kuzindua Doto Cup, Iddi Cup, Saashisha Cup na kubaki maeneo mengine ni Dar es Salaam tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe sana Wizara iweke mfumo mzuri wa kuhakikisha kwamba…

MHE SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Iddi Kassim, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Saashisha.

TAARIFA

MHE SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba ni kweli nchi hii ina vipaji vya wasanii wengi. Pale Jimbo la Hai tuna Jukwaa la Wasanii, wasanii wengi, na Mheshimiwa Naibu Waziri tulikwenda naye, aliona vipaji vikubwa na yeye mwenyewe akashangaa, akauliza hapa ni Hai au tuko wapi. Kwa hiyo ni kweli tuna vipaji vingi Mheshimiwa Waziri washuke watambue vipaji hivi na kuvisaidia, ahsante sana.

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Iddi Kassim, taarifa unaipokea?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo naipokea kwa asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe mfano; tunaye msanii mmoja anaitwa Issa Jim, yupo Kahama. Msanii huyu ni professional boxer, anamiliki mikanda miwili, ameshinda International UBO, anao mkanda huo Kahama; ameshinda pia mashindano ya Afrika Mashariki (WABA); ameshiriki mashindano matano, manne ameshinda moja ametoa draw, yupo Kahama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini toka anaanza kuandaa mashindano haya hakuna support ya aina yoyote ile aliyopewa na wala hatambuliki na wala hata hapa hajaalikwa. Leo tunawaona akina Mandonga wako hapa, lakini kwenye maeneo yetu kule hamuwaaliki. Ni lazima tusimame na tuseme kwamba Watanzania wote tuna haki sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Wizara pelekeni, waelekezeni maafisa utamaduni kwenye maeneo yenu huko kuhakikisha kwamba wanashiriki kuibua vipaji, kusaidia wasanii ili na wao waweze kufika kwenye maeneo haya. Kaka yangu, Mheshimiwa Babu Tale, amesema hapa, Diamond ametokea Kigoma. Leo hii Wana-Kigoma angekuwa Kigoma kule leo tungekuwa tunamhesabu ni mtu wa Kigoma. Tunahitaji tusambaze keki hii kwenye maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana Mheshimiwa Waziri, dada yangu, mhakikishe ya kwamba mnakwenda kuwaelekeza hawa maafisa utamaduni kwenye maeneo yetu ili wafanye kazi. Wasanii hawapewi ushirikiano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho; leo hii utaona ofisi hizi; BASATA, COSOTA, zote ziko Dare es Salaam. Leo hii msanii anayetoka Kata ya Bulyanhulu anaandaa kazi yake. Ili apate kibali maana yake ni kwamba aandae kazi akiwa Bulyanhulu, apande gari aende akapate kibali Dar es Salaam, na mwisho wa siku akirudi huku bado hawa watu wa COSOTA anakuwa hana hati miliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ni lini mkazi wa Bulyanhulu atatoka aende Dar es Salaam kupata kibali; kwa nini msifungue ofisi hizi au mkawakaimisha hawa maafisa utamaduni kwenye maeneo yale ili kuhakikisha kwamba wawasaidie wasanii wetu kule chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama za usafiri, msanii anatoka hana ndugu wala rafiki Dar es Salaam, anajichanga changa anakwenda mwenyewe Dar es Salaam, matokeo yake ni nini, anaingia kwenye mambo mabaya ambayo yatamhatarishia maisha yake. Kwa hiyo niombe sana kwamba wasanii wetu hawa wanahitaji kupewa ushirikiano kwenye maeneo yao hayo ya huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la kodi mbalimbali. Leo hii tumeona ili mtu aandae kibali, tamasha, kwa mfano pale Shinyanga kuna taasisi inaitwa HolySmile. HolySmile yeye mwenyewe amejichanga changa ameamua kuanzisha sasa tuzo mbalimbali, kutafuta ni nani msanii bora na ni nani mwimbaji bora. Lakini ili apate kibali, gharama yake anatakiwa alipe 1,500,000. Hebu punguzeni, pia muone namna ya kupunguza gharama hizi, ni kubwa sana kwa wasanii hawa wa chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mikopo mnayotoa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kassim.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie la mwisho; mikopo hii mnayotoa mnawapa wasanii wakubwa, kwa nini hamuwapi hawa wasanii wanaochipukia huku chini? (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Kassim.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninaunga mkono hoja. Lakini kwa kumalizia ninaomba pia Mheshimiwa Waziri aongee na Kampuni ya Barrick kama alivyosema Mheshimiwa Sanga hapa, waweze kutujengea uwanja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, naunga mkono hoja.
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yangu Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, pia ninampongeza Waziri Kaka yangu Mheshimiwa Nape Nnauye kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, bila kusahau Naibu Waziri ambaye kimsingi mimi kama Mbunge wa Jimbo la Msalala kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Msalala na hasa Kata ya Jana, Kata ya Mwaruguru ndio Naibu Waziri wa kwanza kufika kwenye maeneo haya. Kwa hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo umekuja kuifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natamani nizungumzie habari ya mawasiliano katika Jimbo langu la Msalala na Naibu Waziri nadhani kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, alifanya ziara kwenye Jimbo langu la Msalala kuona hali ya mawasiliano katika maeneo yale. Ni kwamba katika Jimbo la Msalala hali ya mawasiliano ni mbovu sana, minara hakuna, hata kwenye Makao Makuu yetu ya Halmashauri bado Watendaji wanapata taabu sana wnapoenda ku-load document inabidi sasa wasafiri waende Manispaa ya Mji ili kuweza kufanya kazi zao za kimawasiliano. Naibu Waziri aliagiza na akaahidi kwamba atatupatia minara Saba na wananchi wanasubiri na niombe sasa Mheshimiwa Waziri unapokuja kufanya winding up hapa, utueleze ni lini sasa hiyo minara saba ambayo mlitupatia ambayo itakwenda kujengwa kwenye Kata ya Jana, Kata ya Mwaruguru, Kata ya Mwanase bila kusahau Kata ya Lunguye, Kijiji cha Nyangarasa na Kijiji cha Busolega na Kijiji cha Nyamishiga. (Makofi)

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

T A A R I F A

MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninampa taarifa mwongeaji kwamba eneo la Halmashauri ya Msalala pia linafanana sana na Halmashauri ya Ushetu, hata Makao Makuu ya Halmashauri ya Ushetu hakuna mawasiliano kabisa. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Iddi, unapokea taarifa?

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaipokea taarifa hiyo basi nimuombe Waziri tu aweze kuona aipe kipaumbele Wilaya ya Kahama katika Halmashauri hizi, kwa maana ya Halmashauri ya Ushetu lakini special kwenye Halmashauri ya Msalala kwa sababu Halmashauri ya Msalala ndiyo key ya Majimbo yote haya mawili kwa maana ya Jimbo la Ushetu na Jimbo la Kahama Mji. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ninakuomba utakapokuwa unafanya winding up hapa uje utueleze ni lini sasa hawa Wakandarasi watakwenda kuanza kazi ya kujenga minara katika maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafahamu ili uchumi uweze kukua na hasa katika maeneo yetu ambayo tunatoka katika maeneo ya madini, watu wanahitaji kufanya biashara kila siku hivyo wanahitaji mawasiliano, jana nili-share picha moja nikimuonesha bwana mmoja katika Mgodi wa Nyamishiga Kata ya Runguya, ametengeneza kiti kimoja kirefu sana na amekaa juu na watu wamepanga foleni akiwahudumia kupitia simu yake. Hivyo ni kuonesha dhahiri kwamba bado huduma za mawasiliano katika maeneo hayo hazijafika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kuzungumzia habari nzima ya maslahi ya Waandishi wa Habari. Kila mmoja wetu hapa anafahamu kwamba kazi kubwa ambayo inafanywa na waandishi wetu hawa wa Habari; na sisi kama Waheshimiwa Wabunge lakini Viongozi mbalimbali huwatumia hawa waandishi wa habari katika kufanya kazi zetu katika maeneo yale, lakini bado Waandishi wa Habari hawa wamekuwa hawana mikataba ya kudumu. Mheshimiwa Waziri ninakuomba nenda kawalinde waandishi wetu wa habari wanafanya kazi kubwa sana, maslahi yao bado ni madogo mno Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaona kwamba kwenye msafara mmoja unaweza kukuta una Waandishi wa Habari mathalani 20 na wanafanya kazi kubwa kweli, kila unapokwenda wao ndiyo wa kwanza kushuka na wao ndiyo wa kwanza kukimbia kurudi kwenye magari na mwisho wa siku baada ya hapo Mheshimiwa Waziri wanaishia kupewa Shilingi 20,000, Shilingi 30,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri hebu nenda sasa mkaweke mfumo wa kuwalinda hawa Waandishi wetu wa Habari waweze kuwa na mikataba ya kudumu lakini pia waweze kulipwa stahiki zao kwa muda. Nilikufuatilia siku moja alipofariki Mwandishi mmoja wa Habari, ulitoa maelekezo aweze kulipwa haki zake, lakini mpaka ninapozungumza hivi bado hajalipwa haki zake. Kwa hiyo, ninakuomba Mheshimiwa Waziri Waandishi wa Habari hawa ndiyo wanafanya kazi kubwa ya kuhakikisha kwamba, wanatangaza mema yote yanayofanywa na Serikali yetu hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie nizungumzie suala zima la bando. Kuna wizi unaendelea kwenye suala zima la bando, ni kwa nini Mheshimiwa Waziri msitusaidie kwa sababu ukiangalia kilio kikubwa cha wananchi kwa sasa ni bando. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii unakwenda kujiunga bando mathalani ya Shilingi 30,000 na wanakuambia kabisa utapata dakika kwa mfano, 2,500 lakini utapata GB 12, lakini kutokana na hali ya uchumi unajitahidi sasa kujibana uweze kutumia dakika zile vizuri lakini hivyo hivyo unajitahidi kubana utumie MB vizuri, lakini mwisho wa siku inapofika siku 30 hujui zile dakika zimekwenda wapi? Sasa nikuombe utakapokuja kufanya winding up hapo utueleze, hizi dakika ambazo tunazilipia ambayo ni haki yetu ya msingi tumezilipia huwa zinakwenda wapi? Either ni Serikalini au zinakwenda wapi, tufahamu sasa hizi dakika zinazochukuliwa zinakwenda wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kusema hayo ahsante sana, mchango wangu mimi ni mfupi sana kwa siku ya leo. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia fursa ya mimi leo kuchangia. Kwanza kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya, pia ninampongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Naibu Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania bila kumsahau Mheshimiwa Dkt. Tulia Ackson, Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya na kutuwakilisha vema katika Bunge letu hili Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninataka nichangie mambo machache tu kwenye Wizara hii ya Serikali za Mitaa - TAMISEMI. Kwanza kabisa sisi Wanajimbo la Msalala tunazo shukrani nyingi kwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa fedha nyingi sana alizotupatia za maendeleo kwenye Jimbo la Msalala. Ametupatia fedha nyingi kwenye sekta ya afya, tunatakribani ya vituo vipya sita vya afya ametuletea, tuna zaidi ya zahanati 34 zimekamilika lakini juzi nimeenda kukabidhi ambulance mpya kwa niaba ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ambayo itaenda kuhudumia wananchi wagonjwa wa Kata ya Isaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hajaishia hapo kwenye sekta ya elimu ametupa fedha nyingi sana, tuna shule zaidi ya saba mpya, hajaishia hapo ametuongeza fedha nyingine ya kujenga Chuo cha Veta bilioni mbili na chuo sasa hivi kinaenda vizuri sana. Hajaishia hapo ametupa fedha za kujenga Chuo cha Nursing na chenyewe kimekamilika, hivi karibuni tunaenda kupokea wanafunzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya miaka minne, ndani ya miaka mitatu ya Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan tunaenda kuwa na vyuo viwili kwenye Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan anatafuta fedha nyingi sana kwa uchungu mkubwa, kwa wivu mkubwa kuhakikisha ya kwamba wananchi wa Jimbo la Msalala na nchi nzima wananufaika na miradi mbalimbali kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nianze kwa kuunga mkono maazimio haya ya Kamati na nimpongeze sana Mwenyekiti wa Kamati hii kwa maazimio mazuri kabisa, maazimio yenye afya ambayo ninaimani kabisa kama yataenda kutekelezeka basi kutakuwa na mabadiliko makubwa sana kwenye sekta hii ya TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa mimi nakubaliana moja kwa moja na suala zima la mapendekezo ya Kamati ya kupitia upya Kanuni ya uendeshaji wa Mabaraza yetu ili kuona namna gani sasa Waheshimiwa Wabunge wanashiriki vema kwenye shughuli za maendeleo kwenye maeneo hayo. Ukweli usiopingika ni kweli Mheshimiwa Mbunge ni Diwani na ni Mjumbe wa Kamati ya Fedha lakini kiuhalisia huu uhalisia wa Mheshimiwa Mbunge kuwa Mjumbe wa Kamati ya Fedha na kuwa Mjumbe wa Baraza mara nyingi kalenda ya upangaji wa vikao kwenye maeneo hayo hatushirikishwi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Waziri yuko hapo ni namna gani sasa mje na mkakati wa kutoa maelekezo au mwongozo wa kupeleka kule kwenye Halmashauri upangaji wa vikao hivi vya Kamati ya Fedha na Mabaraza uzingatie ratiba ya Waheshimiwa Wabunge kuwepo kule ili tuweze kushiriki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mbunge anakuwa anakuwa vizia Kikao cha Kamati ya Fedha, anavizia Baraza, ukikaa Jimboni muda wote uko Jimboni, lakini ratiba ya Bunge ikitoka tu ukiwa safarini kuelekea Dodoma unapokea message kwamba kesho kuna Kamati ya Fedha, kesho kuna Baraza, hivi wanaogopa nini kutoa ratiba wakati Mheshimiwa Mbunge akiwa yuko Jimboni ili aweze kushiriki kama Mjumbe halali wa Kamati ya Fedha, aweze kushiriki kama Mjumbe wa Baraza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapeleka fedha nyingi sana kule chini na wengi mmeona, ninampongeza Katibu wetu Mwenezi amefanya ziara kwenye maeneo hayo, amekuta changamoto nyingi sana na ninataka niseme na Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu yuko hapo. Mheshimiwa Rais anapeleka fedha nyingi sana kwenye Majimbo yetu lakini wasimamizi walioko kwenye maeneo haya na hasa aliowapatia dhamana, hawatimizi majukumu yao ya kusimamia kazi vizuri, wanamuhujumu kwenye maeneo ya miradi huko chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha zinazokwenda huko nitolee mfano kwenye Jimbo langu mimi, tumepokea fedha nyingi sana. Juzi tumebaini wizi wa fedha kiasi cha shilingi milioni mia mbili na wezi wamekatwa wamekula Fedha za TASAF, wazee ambao hawawezi kufanya shughuli. Mheshimiwa Rais ametafuta fedha amewapelekea hawa akinamama wanyonge kwa ajili ya TASAF lakini baadhi ya watumishi wachache ambao siyo waaminifu wameenda kula zile fedha na nini kimefanyika? Hakuna hatua yeyote iliyochukuliwa isipokuwa ni kwamba kaeni hapa, kila mwisho wa mwezi tutawakata kwenye mshahara wenu laki moja moja. Hivi fedha hizi anazozitafuta Mheshimiwa Rais kwa uchungu, anapeleka huko ili zikawahudumie wananchi, watu baki wanakula fedha na hakuna hatua madhubuti zinazochukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu niiombe Serikali ikiwezekana iweze kutoa mwongozo kwa sasa na hasa kwa kipindi hili tulichopo. Mheshimiwa Rais amewaamini watu kule wasimamie shughuli za maendeleo kule chini, lakini watu hao ni ukweli usiyopingika kwa wakati huu wanatumia gari za Serikali ambazo zingetumika kwenda kutatua migogoro, wanatumia mafuta ya Serikali ambayo yangetumika kwenda kutatua migogoro, wanaanza kwenda kutafuta kura na watu hawa Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu utoke mwongozo wa kuwaambia kama kuna watu ambao wanahitaji kumsaidia kumsaidia Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa sasa wajitokeze kumsaidia kwa ukweli na wale ambao wanawaza kwenda kugombea Majimbo waache kazi zile waende wakagombee Majimbo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanatumia fedha za Serikali, wanatumia magari ya Serikali, wanaenda kuanza kukimbizana na Wajumbe kwenye maeneo hayo, niombe sana Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu, hebu Serikali sasa itoe mwongozo wale watakao taka kumsaidia Dkt. Samia Suluhu Hassan ili miradi iweze kukamilika huko chini. Tunaenda kwenye uchaguzi, miradi mingi haikamiliki na wale wazembe ambao wanakula fedha hatua kali zichukuliwe ili kuhakikisha ya kwamba miradi ile inakamilika. Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu niombe sana hili liweze kuchukuliwa hatua kali ili tuweze kumsaidia Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nizungumzie suala zima la vituo vya afya; siku zote mimi huwa nasema katika uanzishwaji wa vituo vya afya hivi huduma inayotolewa kwenye vituo vya afya mara nyingi hakuna huduma inayotolewa bure ni huduma ya malipo. Huwa najiuliza na mara nyingi huwa nakaa nao kuona kwamba kuna utofauti gani kati ya vituo vya afya (dispensary za private) na vituo vya afya vya Serikali, huduma ni zilezile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali njooni na mkakati wapeni Ma-DMO na in-charge wa kwenye vituo vya afya hivyo kipimo kwamba kipimo cha in-charge kwenye Kituo cha Afya A ni kuhakikisha ya kwamba anakusanya mapato, anasimamia mapato vizuri, pia ahakikishe kwamba dawa zinapatikana wakati wote hiyo inawezekana na ikiwezekana kwa sababu mmeshagatua madaraka yako huko maana yake kwenye mapato lindwa wanaruhusiwa kukusanya mapato na kutumia, waweze basi kuajiri, kwenye vituo vya afya hivyo…

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana, malizia mchango wako, muda wako umeisha.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote wa Mwaka 2022
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza kabisa nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema siku ya leo kuweza kutoa mchango wangu kwenye Huduma ya Bima ya Afya kwa wote. Moja kabisa nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais, Daktari Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya kwenye nchi yetu hii ya Tanzania na hasa kwenye Mkoa wa Shinyanga Wilaya ya Kahama Halmashauri ya Msalala. Mheshimiwa Rais ametufanyia mambo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Sekta ya Afya Mheshimiwa Rais, Daktari Samia Suluhu Hassan ametuletea fedha nyingi sana ambazo zimeenda kujenga Miundombinu ya Afya na Naibu Waziri, Daktari Mollel atakuwa shahidi alipokuja kutembelea kwenye Jimbo la Msalala na tukafanya ziara ambapo alishuhudia Ujenzi wa Zahati zaidi ya thelathini na nne zikiwa zimekamilika kwenye Jimbo la Msalala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nichukue fursa hii pia kumpongeza sana Dada yangu Ummy anafanya kazi kubwa sana. Nichukue fursa hii kukupongeza Dkt. Mollel unafanyakazi kubwa sana na wewe utakuwa shahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Msalala Halmashauri ya Msalala tumeweza kupatiwa fedha za kujenga Vituo vya Afya zaidi ya vinne. Hivyo kupelekea kuwa na jumla ya Vituo vya Afya kumi kwenye Jimbo la Msalala. Mheshimiwa Rais kwa kushirikiana na Mgodi wa Barrick wameweza kutupatia fedha, tukaweza kukamilisha Zahati ishirini na nne na zingine tukaongeza Zahanati kumi na kwa sasa tumekamilisha zaidi ya Zahati thelathini na nne. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme kwanza kabisa ninaunga mkono, tunaunga mkono sisi Wanamsalala ni wahitaji wa Bima ya Afya kwa Wote ni wahanga. Kwa hiyo Dada yangu Ummy Mwalimu tambua ya kwamba, Jimbo la Msalala tuko pamoja na wewe tuko pamoja na Mheshimiwa Rais. Tunaunga mkono, mwenyewe Mbunge nimefanya ziara tayari nimewaelimisha wananchi na sasa tunasubiria usichelewe, tunahitaji Huduma ya Afya kwa Wote iweze kufanyiwa kazi haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye Jimbo la Msalala kwa sasa kila Kijiji takribani Zahati zimekamilika na Zahati zote hizi ishirini na nne zimekamilika sasa baadhi ya Zahati bado hatujazifungua kwa nini hatujazifungua? ni kwa sababu ya kukosa Watumishi na kukosa Vifaa tiba. Hivyo niombe, tunapoenda kupitisha sheria hii basi Mheshimiwa Waziri ni muhimu sana mkatupa jicho la pekee kwenye Jimbo la Msalala. Kwa sababu tayari Zahati ishirini na nne zimekamilika na hazijafunguliwa, zinahitaji Watumishi, zinahitaji Vifaa Tiba hivyo tunaomba basi muende mkahakikishe ya kwamba vifaa tiba na Zahati hizi zinaenda kufunguliwa na zinafanya kazi ili ziweze kutoa huduma kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi kwenye Jimbo la Msalala tuna Vituo vya Afya ambavyo vinafanya kazi. Nichukulie mfano vituo viwili tu ambavyo vimekuwa na changamoto kubwa sana ya juu ya upatikanaji wa Bima za Afya na huduma kwenye maeneo yale. Tuna Kituo cha Afya Bugarama, tuna Kituo cha Afya Runguya kumekuwa na changamoto nyingi na kubwa sana juu ya upatikaji wa huduma kwa wananchi wetu, hasa wale wenye bima zile za awali. Hivyo naamini baada ya kuwa tumeenda kupitisha huduma hii ya afya kwa wote itaenda kuondoa tatizo la rushwa kwenye maeneo yale, itaenda kuondoa tatizo la kutopatiwa huduma kwa wakati, kwa wananchi wetu kwenye maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwani tumepata changamoto kubwa sana na haya ndiyo malalamiko ya sisi wananchi wetu kwa Wabunge kwenye maeneo yetu yale kumekuwa na huduma mbovu. Kwa sababu tu mtu akienda na fedha yule mwenye bima haudumiwi kwa wakati, anawahudumia kwanza mwenye fedha na ile fedha namna ya kuweza kui-manage inakuwa ni kazi ngumu sana matokeo yake ile fedha inaingia mifukoni mwa watu na haiendi kutatua tatizo la kununua dawa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe ninaamini kabisa Uanzishwaji wa Huduma ya Bima hii itaenda kusaidia upatikanaji wa madawa, itaenda kusaidia upatikanaji wa huduma kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilifanya ziara siku moja kwenye Kituo cha Afya Runguya, nikawaeleza wahudumu na madaktari kwenye eneo lile, nikasema, ni lazima ifikie wakati sasa watumishi na Madaktari kwenye maeneo yale wanaofanya kazi kwenye Vituo vya Afya na Zahanati zetu waondoe mentality za kufanya kazi Kiserikali na wafanye kazi Kibiashara kwani huduma zinazotolewa kwenye maeneo yale ni huduma za kibiashara. Hivyo, ni bora wakakaa wakatengeneza mpango kazi mzuri utakaowawezesha kukusanya mapato vizuri, kutoa huduma zilizokuwa bora na upatikanaji wa dawa kwenye maeneo yale.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo changamoto dada yangu Ummy uende ukazifanyie kazi, hasa katika kuboresha upatikanaji wa dawa na hii MSD.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maeneo yetu hasa ya vijijini na hasa sisi kwenye maeneo ya wachimbaji kumekuwa na changamoto kubwa gari za MSD zinapoleta dawa. Unakuta gari kubwa limeleta dawa lakini linapofika pale linatushushia mipira mingi ya kujikinga kuliko dawa. Niombe, tunapokwenda kutekeleza huduma hii na mpango huu, kuhakikisha kwamba madawa yanaenda kupatikana. Shirika hili liende likaboreshwe na waache kutuletea mipira ya kinga kwa wingi, walete dawa ambazo zitasaidia wananchi wetu waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Ummy. Lakini niombe, Mheshimiwa Mollel unafahamu, tumeanzisha chuo ambacho tumepewa fedha na Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kushirikiana na Mgodi wa Barrick tumemaliza Chuo cha Afya. Niombe Mheshimiwa Waziri uje tuweze kukifungua chuo kile ili mwaka kesho kianze kutoa huduma ili tupate watumishi waende wakahudumie kule na huduma za afya kwa wote zinapokuja kuanzishwa basi ziende zikatoe huduma vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi sina mengi, naomba niwapongeze sana. Usichelewe dada yangu Ummy, anza kutekeleza mapema. Wananchi wa Msalala tuko nyuma yako Mheshimiwa, tunahakikisha ya kwamba huduma hii inaenda kufanya kazi vizuri. Kwani, mnafahamuu mimi mwenyewe maombi niliyokuwa nayo, kuna watu wako ndani wana magonjwa sugu hatuwezi kuwahudumia. Leo hii Mbunge nimekuwa nikipokea maombi mengi, watu wanataka fedha za operesheni, wanataka fedha za kwenda kufanyiwa ultrasound. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Samia Siluhu Hassan, ametuletea fedha zaidi ya milioni 750 tumeleta vifaa, ultrasound, X-ray ziko kwenye maeneo yale. Sasa ziende zikafanye kazi, tuleteeni wataalamu wa kutosha ili huduma ya Bima ya Afya kwa wote hii itakapoanza basi iweze kuhakikisha kwamba inatoa huduma…

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Mbunge wa Msalala. Pamoja na kupewa hizo fedha za vifaa tiba na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, leo halmashauri zote tumepewa fedha kwa ajili ya ukarabati wa Hospitali zetu za Wilaya, ahsante sana. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Ahsante kwa taarifa, haya tunaendelea.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ninapokea taarifa hii kwa mikono miwili kwani ndio utaratibu wa Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuhakikisha ya kwamba anatuletea fedha kuweza kukamilisha miundombinu ya afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimalizie kwa kukushukuru sana Mheshimiwa Ummy, chapa kazi. Ninaunga mkono hoja kwa asilimia 100, wana-Msalala tuko pamoja na wewe. (Makofi)