Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Stephen Lujwahuka Byabato (316 total)

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Waziri kwa majibu yake mazuri. Kwa kuwa mradi wa REA utaanza Februari hii ambapo leo ni tarehe 3 na katika Jimbo la Lushoto kuna vijiji vimerukwa kwa muda mrefu sana hasa katika Vijiji vya Kilole, Ngulu, Gale, Miegeyo, Handei, Magashai, Tambwe, Mazumbai, Ngwelo, Milungui na kata nzima ya Makanya. Je, Serikali haioni kwamba sasa vijiji hivi lazima vipewe kipaumbele kwa ajili ya kupata umeme kwa sababu wamesubiri kwa muda mrefu sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Jimbo la Lushoto lina vitongoji zaidi ya 32 na Mheshimiwa Waziri Kalemani yeye ni shahidi ametembelea Lushoto na akaona Wilaya nzima ya Lushoto hakuna nyumba ya nyasi hata moja na wananchi wote wameshafanya wiring wanasubiri umeme. Je, ni lini sasa vitongoji vile vya Wilaya ya Lushoto vitapata umeme kwa wakati ili wananchi wapate huduma stahiki kama wenzao wanavyopata huduma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, commitment ya Serikali ni kwamba, ifikapo tarehe 15 Februari, 2021 vijiji vyote vilivyobakia 2,150 ambavyo havikuwa vimepata umeme katika REA Awamu I, II na III mzunguko wa kwanza vitapelekewa umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliofanyika sasa hivi ni kuhakikisha kwamba mkandarasi mmoja hapewi kazi kubwa sana. Kwa hiyo, tutaona maajabu makubwa katika kipindi hiki ambapo tutaanza kupeleka umeme katika maeneo mengi kwa wakati mmoja kwa sababu mkandarasi mmoja pengine inaweza ikawa anapeleka umeme au jimbo moja. Kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Shekilindi, kwamba huduma anayotupatia ya dawa na sisi tutapeleka huduma ya umeme kwenye kwa kadri tulivyoelekeza katika kipindi hiki hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili la kupeleka umeme kwenye vitongoji, Wizara ya Nishati kwa maelekezo ya Serikali inatekeleza mradi unaoitwa densification na sasa tuko katika densification 2B ambao ni mradi jazilizi kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji na kufikia mwezi Mei tutakuwa tayari tumesaini mikataba kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji zaidi ya 2,800 katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa hiyo, tunaamini katika upanuzi huo wa miradi jazilizi, basi Jimbo la Lushoto pia litapata maeneo kadhaa ya kuwekewa umeme katika maeneo ya vitongoji vyake. (Makofi)
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, katika vitongoji 514 vilivyoko Jimboni Ukerewe vitongoji 238 bado havina umeme, lakini hata vile vitongoji 276 ambavyo tayari vina umeme, umeme wake unakuwa una matatizo makubwa, umeme unakatika mara kwa mara kwenye Jimbo la Ukerewe na hii inatokana na cable inayosafirisha umeme kutoka Kisorya kwenye Lugezi kuchoka.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua sasa Serikali ina mpango gani ili kuweka cable nyingine mpya iliyo sahihi ili kurekebisha hali hiyo na kusababisha wananchi wa Ukerewe kupata umeme wa uhakika?

Lakini swali langu la pili, kupitia mradi huu wa REA Serikali iliingia mkataba na makampuni binafsi kusambaza umeme kwenye maeneo ya visiwa, baadhi ya makampuni yalifanya kazi muda mfupi lakini hayakukamilisha kazi kwenye baadhi ya visiwa kwa mfano Visiwa vya Ghana, Visiwa vya Bulubi; makampuni yalisimika nguzo lakini wananchi hawakuweza kupata umeme. Lakini baadhi ya visiwa makampuni yalitowa umeme kwa mfano Kisiwa cha Ukala, Kisiwa cha Ilugwa lakini umeme ule ukawa unauzwa kwa bei ghali na baada ya Serikali intervene gharama ile ilishuka lakini wananchi wakawa wanapata umeme kwa mgao.

Nini kauli ya Serikali sasa ili iweze kutoa faraja kwa wananchi wa maeneo haya ya Visiwa vya Ukerewe? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, jimbo la ukerewe ni moja wapo majimbo ambayo yako katika miradi ni jimbo linalopata umeme kwa miradi ya TANESCO ya Gridi na miradi ya off grid. Kwa hiyo ni kweli kwamba kuna tatizo la umeme ambalo linafahamika katika maeneo ya Ukerewe na hasa shida ni kama alivyosema kwamba hiyo kebo inayopeleka umeme kule imekuwa ikipata matatizo.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ukerewe linapata umeme kutoka sub station yetu ya Kibara iliyopo pale Bunda na umeme ukitoka pale unasafirishwa kwa waya za kawaida kuelekea kisolia baada ya Kisorya unaenda kupitia kwenye maji kwenda Igongo na baada ya Igongo unaingia Lugezi ambacho ni kisiwa chenyewe cha Ukerewe. Kutoka Bunda kwenda mpaka Igongo siyo shida tena, lakini kutoka Igongo kwenda mpaka Lugezi kuna mita 700 ambapo ndiyo sasa ile cable inayopitisha umeme inapita majini na imekuwa ikipata shida kwa sababu siyo ile cable ambayo inatakiwa kupita kwenye maji.

Mheshimiwa Spika, tayari Serikali kupitia TANESCO imeshaanda mazingira ya kufanya njia ya muda mfupi na njia ya muda mrefu ikiwa ni pamoja na kuhakikisha kwamba basi inawekwa sub-marine cable kwa hizo mita 700 kuhakikisha kwamba sasa umeme utakuwa ni wa uhakika kwa Jimbo la Ukerewe.

Mheshimiwa Spika, shida nyingine iliyokuwepo ni kwamba nguzo ambazo zimekuwa zikishikilia umeme kwenye eneo la Igongo nguzo zinazotembea kwa kilometa angalau moja zimekuwa zikijaa zikiingia kwenye maji kwa hiyo zinaharibika kwa hiyo mradi wa muda mfupi tutaweka pale nguzo za zege kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mradi wa umeme unaweza kuwa wa uhakika kwenye jimbo letu la Ukerewe. Lakini njia ya muda mrefu inayotarajiwa kufanyika kuanzia mwezi Januari mwakani itakuwa ndiyo hiyo hiyo ya kuweka marine cable ambayo itaanzia kutoka Jimbo la Bunda pale kwenda mpaka Ukerewe itakuwa ni mradi wa uhakika ambao utafikisha sasa umeme kwenye jimbo letu la Ukerewe bila wasiwasi wowote na tunatarajia labda mwakani ndiyo serikali itajipanga kutekeleza mradi huo ambao utagharimu takribani bilioni 12.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili kuhusiana na wale wanaopeleka umeme ambao walikuwa siyo wa TANESCO. Serikali kupitia REA ilipata watu wakandarasi mbalimbali wa kupeleka umeme kwenye maeneo ambayo Gridi ya Taifa haijafika na umeme wa jua tunaita nishati mbadala, nishati jadidifu. Ni kweli kwamba maeneo ya ukerewe na maeneo mengine ya visiwa vilivyopo Muleba na Geita vimekuwa vikipata shida ya bei na shida kubwa ya bei ilisababishwa na wakandarasi waliotengeneza hiyo miradi kuwa na gharama kubwa ya uuzaji wa umeme kuzidi kile kiwango ambacho TANESCO inakielekeza.

Mheshimiwa Spika, TANESCO inauza unit moja kwa shilingi mia moja lakini wenzetu walikuwa wanauza unit moja hadi kufikia shilingi 3,500 na Serikali Mheshimiwa Waziri Mkuu alielekeza mwaka jana kwamba gharama hizo zishuke kuja kwenye gharama ambazo ni za kawaida ili kuepusha kuwa na gharama ya double standard kwenye maeneo yale yale ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, tunavyofahamu ni kwamba maelekezo hayo yalitelekezwa kama alivyosema Mheshimiwa Mkundi lakini yale maeneo mbayo bado maelekezo hayo hajatekelezwa basi tunaomba taarifa hizo zifikishwe ili tuweze kuchukuwa hatua.

Mheshimiwa Spika, lakini pia wazabuni hawa ambao walikuwa wanatoa umeme huo tumekuwa tukizungumza nao na majadiliano yanaendelea na tutahakikisha kwamba wanaendelea kupeleka umeme wa uhakika kwa gharama nafuu na kuwafikia wateja wote muda wote ili adhima ya Serikali ya kufikisha umeme kwa ajili ya maendeleo ya viwanda kuwa salama yaweze kufikiwa.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri Nishati lakini nina swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, halmashauri ya Wilaya ya Uyui hasa Jimbo la Igalula tuko nyuma sana katika kuunganishiwa nishati ya umeme. Wakati wa kampeni Mheshimiwa Waziri alikuja tukazindua mradi mkubwa lakini mara baada ya kuondoka yule mkandarasi hakuendelea na kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali itaanza utekelezaji wa kupeleka umeme kwenye kata zaidi ya sita zilizoko katika Jimbo la Igalula na vijiji vyake? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, ni lini Serikali itakamilisha mradi wa umeme jazilizi katika vijiji vya kata ya Goeko Msasani, Igalula Stesheni na Kigwa Majengo Mapya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Protas Venant wa Jimbo la Igalula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye jibu la msingi kwamba vijiji vyote 46 vilivyobaki katika Jimbo la Igalula vitapatiwa umeme kuanzia mwezi Februari kwa miezi 18 kwenye mradi wa REA III mzunguko wa pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili ambalo nadhani ndilo la nyongeza alikuwa anasema kwamba mwaka jana Mheshimiwa Waziri alizindua mradi wa umeme jazilizi (Densification) awamu ya pili, Densification 2A.

Mheshimiwa Naibu Spika,Jimbo la Igalula, Mkoa wa Tabora ni mojawapo ya mikoa 9 inayonufaika na Densification 2A ambayo ilianza mwaka jana na tayari ilishazinduliwa kwa Mkoa wa Tabora. Mkandarasi anayefanya kazi katika Mkoa wa Tabora anayo Lot moja ambayo ina mikoa miwili; Tabora na Singida na atafanyakazi hiyo kwa shilingi bilioni 9.7. Tayari mobilization imeshaanza, ameshafanya survey katika Jimbo la Igalula na amekamilisha na tunatarajia muda wowote kufikia mwezi wa nne atakuwa tayari ameanza kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge kwamba amekuwa akifuatilia hata ofisini kuulizia Densification 2A itaanza lini kwenye Jimbo lake, tunamhakikishia kabla ya mwezi Aprili upelekaji wa umeme kwenye vitongoji vilivyoko katika Jimbo la Igalula utakuwa umeanza.
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Wizara, ninayo maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, wakati wananchi wa Muleba wakisubiria hizi hatua ambazo Wizara inazichukua, je, Serikali iko tayari kuiongezea nguvu Ofisi ya TANESCO iliyopo kwa sasa kwa kuiongezea wafanyakazi na vitendea kazi ili wakati tunaendelea kusubiria iendelee kutoa huduma stahiki kwa wananchi wa Wilaya ya Muleba? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Wilaya ya Muleba inavyo visiwa 39 na kati ya hivyo, visiwa 25 vinakaliwa na wavuvi ambao wanachangia pato la taifa. Je, Wizara na Serikali ni lini itavipelekea umeme wa uhakika na wa bei nafuu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TANESCO imeendelea kutoa huduma kwa wananchi na kuhakikisha kwamba huduma ya umeme inapatikana kwa uhakika. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Muleba Kaskazini kwamba tutaendelea kupeleka huduma ya umeme kwa wananchi na kuhakikisha kwamba ofisi ya TANESCO Muleba lakini na maeneo mengine yote nchini zinafanya kazi vizuri kabisa. Serikali tayari imeshaongeza nguvu kazi katika maeneo mbalimbali kwa kupeleka watumishi na vifaa mbalimbali ikiwemo vitendea kazi na magari. Tunaahidi kwamba tutaendelea kuboresha utendaji katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, kama nilivyokuwa nimetangulia kusema kwamba miradi inayopeleka umeme visiwani ni miradi inayoitwa off grid, maeneo ambapo Gridi ya Taifa haijafika na Muleba ni mojawapo ya maeneo ambayo ina visiwa vingi vinavyokaliwa na watu vinavyohitaji kupata huduma ya umeme. Tayari wako watu ambao walikuwa wanapeleka umeme huko ikiwemo kampuni ya JUMEME lakini gharama yake ilikuwa ni kubwa na Serikali ilitoa maelekezo kwamba gharama hiyo ya unit 1 kwa Sh.3,500 ishuke na kufikia shilingi
100. Maelekezo hayo tayari yameshaanza kutekelezwa. Kama bado kuna tatizo katika maeneo hayo basi tunaomba taarifa hiyo itolewa ofisini ili tuendelee kusimamia vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini Serikali inao mpango wa kufikisha umeme wa TANESCO katika maeneo hayo kwa kadri bajeti itakavyoruhusu au kuweza kusimamia ile miradi ili iweze kutoa umeme wa uhakika na kwa gharama nafuu kwa wananchi wote wanaoishi visiwani.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lengo la Serikali ni kupeleka huduma kwa wananchi. Tatizo lililojitokeza hapa ni baadhi ya vitongoji hasa katika Mji wa Kakonko kurukwa. Mfano, vitongoji vya Itumbiko, Mbizi, Kizinda, Cheraburo zikiwemo taasisi kama shule za makanisa. Kwa nini taasisi na vitongoji hivi vinarukwa? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, lini sasa haya maeneo ambayo yamerukwa yatapewa huduma hiyo ya umeme? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aloyce Kamamba, Mbunge wa Kakonko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vitongoji vya Jimbo la Kakonko havijarukwa isipokuwa Serikali inaendelea kupeleka umeme katika vijiji na vitongoji vyetu kwa awamu. Kwa hiyo, kadri ya upatikanaji wa fedha vitongoji vimekuwa vikipatiwa umeme kulingana na mazingira yalivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari umeme umepelekwa katika vijiji 40 vya Jimbo la Kakonko na wakati tunapeleka umeme katika vijiji hivyo baadhi ya vitongoji vilifikiwa katika awamu ya pili ya REA na awamu ya tatu mzunguko wa kwanza. Sasa awamu ya tatu mzunguko wa pili itapeleka umeme katika vijiji lakini na baadhi ya vitongoji pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Kakonko lipo katika awamu ya pili (b) ya mraji jazilizi wa umeme katika vitongoji. Jumla ya vitongoji 49 vitapatiwa umeme katika Jimbo la Kakonko na mradi huu wa jazilizi unaanza kuanzia mwezi Aprili. Kwa hiyo, kadri ya upatikanaji wa fedha, vitongoji vya Jimbo la Kakonko lakini na vitongoji vingine vingi nchini vitaendelea kupelekewa umeme taratibu ikiwa ni pamoja na taasisi za umma. (Makofi)
MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na shukrani kwa Serikali kwa kufungua wilaya ya TANESCO pale Chanika na kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Nishati kwa kufanya ziara kwenye Jimbo la Ukonga, je, Serikali inawaeleza nini wananchi wa Jimbo la Ukonga ambao mpaka sasa miradi yao ya REA haijakamilika kwenye Kata za Chanika, Zingiziwa, Msongola, Majohe na Kivule? Serikali inatoa tarehe gani wananchi wategemee mradi huu kukamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jerry, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema awali kwamba miradi ya umeme ya REA awamu ya tatu mzunguko wa pili itaanza mwezi huu wa pili na itakamilika kufikia Septemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme kwa ujumla kwamba miradi yote ya kupeleka umeme vijijini kwa vijiji 2,150 vilivyokuwa vimebakia havijapata umeme, vyote vitapatiwa umeme katika awamu hii ya tatu mzunguko wa pili ya REA. Baada ya hapo hatutarajii kuwa na kijiji chochote ambacho kitakuwa hakina umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwasihi Waheshimiwa Wabunge waendelee kuwa watulivu na wajiandae kupokea mradi mkubwa wa kupeleka umeme vijijini ambao utakuwa unakmilisha vijiji vyote ambavyo vilikuwa havijapata umeme.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwanza naomba niipongeze Serikali Kuu kwa kazi nzuri inayoifanya ya kutusambazia umeme. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa wananchi wa Namtumbo nyumba zao na taasisi wamefanyakazi yao nzuri ya wiring, lakini wanacheleweshewa kuunganishiwa umeme hususan kijiji cha Mbimbi na Taasisi ya Hunger Seminary na Shule ya Sekondari ya Msindo.

Je, Serikali inaweza kuielekeza TANESCO waharakishe uunganishwaji wa umeme katika vijiji na taasisi hizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa mazingira ya Namtumbo maeneo mengi yana mchwa na yanasumbua sana nguzo za umeme zisizokuwa treated vizuri. Je, Serikali inaweza kuelekeza namna bora ya ku-treat nguzo zinazowekwa au kuwekwa nguzo rafiki na mazingira ya mchwa ya Namtumbo na kwingineko ili kuepuka hasara inayoweza kujitokeza katika mradi huu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vita Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Namtumbo ni mojawapo ya Wilaya ambazo zilikuwa zinapelekewa umeme katika awamu ya tatu mzunguko wa kwanza wa REA. Kilichotokea ni kwamba baada ya kufanyika kwa kazi ya awali wakandarasi waliowengi waliongezewa kazi za nyongeza katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuwafikia wananchi walio wengi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Namtumbo imekuwa ni mojawapo kati ya maeneo ambayo yameongezewa maeneo ya nyongeza na hivyo kushindwa kukamilisha kazi iliyopangwa kwa wakati. Mkandarasi ambaye alikuwa anafanyakazi katika Mkoa wa Ruvuma NAMIS Cooperate ameongezewa muda wa kukamilisha kazi katika mkoa huo mpaka kufikia mwezi Aprili na katika Wilaya ya Namtumbo tayari ile kazi iliyokuwa imeongezeka nguzo zimesimikwa, waya zimepelekwa na kilichobaki sasa ni upatikanaji wa mita kuweza kuwafikishia huduma wale wote waliopelekewa umeme. (Makofi)

Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Vita kwamba ifikapo mwezi Aprili tayari wale wote waliounganishiwa umeme watakuwa wamewashiwa umeme katika maeneo yao bila kuchelewa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili alitaka kujua uwezekano wa kuweka miundombinu itakayokuwa rafiki na ya uhakika katika maeneo ambayo tayari yana matatizo mbalimbali. Tunafahamu na sasa ni maelekezo ya Wizara kwamba katika yale maeneo ambayo oevu kwa maana ni maeneo yenye majimaji, katika maeneo ya hifadhi na katika maeneo yenye matatizo mengine na changamoto kama hizo za miti kuliwa na mchwa tumeelekeza kwamba wenzetu wa TANESCO na REA basi watumie nguzo za zege zinaitwa concrete polls ili kuhakikisha kwamba tukiziweka basi zinakuwa za kudumu na zinakaa kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini niongezee kwamba kwa sababu Waheshimiwa Wabunge wanayafahamu maeneo yao yana matatizo gani, basi maelekezo ya Wizara ni kwamba wale wakandarasi watakaoenda kufanyakazi katika Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili wa REA wahakikishe wanawasiliana pamoja na mamlaka nyingine watakazoziona kwa maana ya TANESCO kupeleka …. kwa Mkuu wa Mkoa, Mkuu wa Wilaya lakini pia wafanye consultation kwa Waheshimiwa Wabunge ili waweze kutoa maoni yao na ushauri wao maeneo gani yanaweza yakafanyiwa nini hata kama siyo ya kitaalam lakini yakichanganywa na ya kitaalam yatatusaidia kuhakikisha miundombinu yetu inadumu katika maeneo husika. (Makofi)
MHE. FRANCIS I. MTINGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuniona naomba niulize swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa changamoto zilizoko Namtumbo zinafanana kabisa na changamoto zilizoko Mkalama hasa Kata ya Mwanga ambayo haikuwahi kupata umeme kabisa katika awamu zote. Je, Serikali inatoa kauli gani kuhusu kata hii ambayo imekuwa ikiutizama tu umeme huu wa REA katika kata nyingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Mkalama kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika,kama tulivyokwishasema kwamba katika Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili wa REA, tutapeleka umeme katika vijiji vyote Tanzania vilivyobaki bila kupata umeme ambavyo hesabu yake ilikuwa ni 2,150. Kazi hiyo itaanza mwezi huu wa pili na tunahakikisha kwamba kufika mwezi Septemba, 2022 vijiji vyote vilivyopo nchini Tanzania vitakuwa vimepata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, niongezee kwamba tunapopeleka umeme vijijini, kimsingi tunapeleka kwenye Mkoa, Wilaya, Kata, vijiji halafu Vitongoji. Kwa hiyo, kuna vitongoji ambavyo pia vitanufaika na awamu ya tatu, mzunguko wa pili wa upelekaji wa umeme kwenye mradi huo ambao utaanza mwezi huu na kukamilika kufikia mwezi Septemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, namhakikishia Mheshimiwa Mbunge wa Mkalama kwamba vijiji hivyo vilivyopo katika kata hiyo, vitapatiwa umeme kwa uhakika.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nafahamu Serikali inatekeleza Mpango wa peri-urban kuhakikisha vijiji vilivyopo ndani ya majiji navyo vinapatiwa umeme. Naomba kujua ni lini Serikali itaweka wazi ratiba yake ili na vijiji vilivyopo ndani ya Jiji la Tanga vitapelekewa umeme huo wa REA? Nashukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwanaisha, Mbunge wa Tanga kwa kueleza kwanza kidogo kwamba Serikali yetu kupitia maelekezo yanayotolewa na Mheshimiwa Dkt. John Joseph Pombe Magufuli, imekuwa ikipeleka umeme katika maeneo mbalimbali kwa taratibu tofauti tofauti.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunao Wakala wa Umeme TANESCO ambao una jukumu na wajibu wa kuhakikisha wanapeleka umeme katika maeneo yote ya mjini na vijijini kwa maana ya kwamba ile miradi inayowekwa katika mazingira fulani, ikishakamilika, basi TANESCO wanaendelea kupeleka umeme katika maeneo hayo. Hata hivyo, tumekuwa na hizo REA I, REA II na REA III; pia tumekuwa na kitu kinaitwa densification (Mradi wa Umeme Jazilizi); vile vile iko hiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameisema ya peri- urban ambao ni mradi unaopeleka umeme katika maeneo ya mijini lakini yenye asili au uonekano wa vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa peri-urban ulianza kwa kupeleka umeme katika Majiji ya Arusha, Mwanza, Dar es Salaam, Mbeya na Dodoma na awamu ya kwanza imeelekea kukamilika, itakamilika mwezi wa nne mwaka huu na baada ya hapo sasa tutaingia katika awamu ya pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba awamu ya pili itakapoanza basi Waheshimiwa Wabunge wote watafahamishwa na wale wote ambao ni wanufaika watapata nafasi hiyo. Pia nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo ya peri- urban bado yanapelekewa umeme na Wakala wa Umeme TANESCO kwa kuzingatia kwamba ni jukumu lake kuhakikisha kwamba anapeleka umeme katika mazingira yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kuwa taarifa itapatikana na ratiba kamili itafahamika. (Makofi)
MHE. REUBEN N. KWAGILWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza ili yaweze kupata majibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; kwa kuwa Wilaya ya Handeni ina majimbo mawili ya uchaguzi na mimi ni muwakilishi wa Jimbo la Handeni Mjini, je, Serikali haioni haja ya kuongeza wigo wa idadi ya viijiji ambavyo havijapata umeme upande wa Handeni Mjini hasa katika Kata ya Mlimani Konje, Kideleko kwa Magome, Kwenjugo, Kwadyamba, Malezi na Mabada?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kumekuwa na hali ya kukatika katika kwa umeme kila mara hali inayopelekea kuwapatia hasara wananchi kwa vyombo vyao vya umeme lakini vilevile kushindwa kufanya shughuli zao za kiuchumi za uzalishaji. Ni lini Serikali itakomesha tatizo hili wananchi wa Handeni Mjini washiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Mbunge wa Handeni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya tatu, mzunguko wa pili wa REA unapeleka umeme katiika vijiji vyote Tanzania Bara ambavyo havikuwa na umeme ambavyo mpaka sasa havizidi 1974. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vijiji vyake vyote ambavyo havikuwa na umeme vitapata umeme katika awamu hii ya tatu, mzunguko wa pili ambayo imeanza tayari mwezi wa nne huu na itakamilika kufikia Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, hilo linaenda pia kwa Waheshimiwa Wabunge wengine wote wa Tanzania Bara, kwamba vijiji vyote ambavyo havikuwa vimepata umeme vimeingizwa katika awamu ya tatu, mzunguko wa pili na tutahakikisha tunapeleka umeme katika maeneo yote hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, ni kweli, Tanga kama Mkoa na Handeni ikiwemo imekuwa na matatizo ya kukatika kwa umeme ikiwemo Mikoa wa Mbeya Pamoja na Mkoa wa Kagera. Hata hivyo Wizara kwa kushirikiana na TANESCO imechukua juhudi mbalimbali kuhakikisha inamaliza tatizo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa Mkoa wa Tanga na hasa Handeni tatizo kubwa lilikuwa ni miundombinu chakavu ambayo ilikuwa inapelekea umeme katika maeneo hayo; na hivyo yamefanyika mambo mawili moja ni la sasa na lingine ni la muda mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, umeme unaokwenda Handeni unatokea katika kituo chetu cha Chalinze unakwenda kwenye substation ya Kasija, unatoka Kasija unakwenda Korogwe – Handeni – Kilindi, na njia ndefu sana ina km. zaidi ya 500. Kwa hiyo, tumebaini kuna nguzo zaidi ya 1300 ambazo zilikuwa zimeoza zimeanza kufanyiwa marekebisho na kuondolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka tunavyoongea sasa tayari nguzo zaidi ya 500 zimerekebishwa, na tumehakikisha kwamba kufikia mwishoni mwa mwezi wa nne, nguzo zote 1300 zitakuwa zimerekebishwa na kuhakikisha kwamba basi umeme haukatiki hovyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika hatua ya pili ambayo ni ya kudumu na ya muda mrefu tumeshauriana na kukubaliana na wataalam, tumekubaliana tujenge kituo kidogo cha kupoza umeme pale Handeni. Kwa hiyo tutatoa umeme Kasija kwenye kituo cha kupoza umeme cha sasa tutapeleka Handeni, km. 81 kwa gharama ya shilingi bilioni 4nne. Tukishajenga kituo hicho cha kupoza umeme pale Handeni basi tutatoa line moja ya kuhudumia Handeni, tunatoa line moja kwenda Kilindi na line nyingine moja itaenda kwenye machimbo ambayo tumeambiwa itaanzishwa siku si nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo tunahakikisha kwamba basi tatizo la kukatika umeme Wilaya yetu ya Handeni na majimbo yote mawili litakuwa limefikia ukomo na tutakuwa tuna uhakika wa umeme.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri hapo umetoa maelezo marefu na mimi ninakupongeza sana. Sasa hapo umeitaja Mbeya halafu kule hujaeleza tatizo ni nini, maana huko kwingine umesema ni nguzo haya Mbeya unakatika katika kwa nini?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nilipoitaja Mbeya nikaitaja Kagera kwasababu na mimi natokea Kagera ili utakaponipa nafasi ya kuzungumzia Mbeya basi na Kagera nipitie humo humo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mbeya tunayo matatizo makubwa mawili, tatizo moja kubwa ni radi ambazo zimekuwa zikisumbua mifumo yetu ya umeme kwenye transfoma. Tatizo hilo pia liko Mkoa wa Kagera. Tulichokifanya katika mikoa hii miwili tumeanza kufunga vifaa vinaitwa auto recloser circuit breaker ambayo vinazuia radi isirudi kwenye maeneo mengine ambayo hayajaathirika hilo ni tatizo moja kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tatizo la pili lilikuwa ni uchakavu wa miundombinu kwenye maeneo hayo. Tumeunda vikosi kazi maalum katika mikoa hiyo mitatu, Mbeya, Tanga na Kagera ya kuhakikisha kwamba kinapitia kila eneo na kubaini tatizo kubwa ni nini ili iiweze kurekebisha. Vikosi kazi hivyo viko kazini, vinafanya kazi; na tunahakikisha kufikia mwezi wa sita, maeneo yote ambayo yalikuwa yana matatizo sugu yatakuwa yamefanyiwa kazi na kurekebishwa.
MHE. RASHIDA A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Matatizo ya usambazaji wa umeme vijijini yaliyopo Handeni ni sawa kabisa na yaliyopo kule Lushoto katika Jimbo la Mlalo. Hivi ninavyozungumza tunapoelekea kwenye robo ya tatu ya mwaka wa fedha ambao unakaribia kwisha hakuna hata kijiji kimoja ambacho REA wamesambaza umeme. Sasa tunataka kujua, wananchi wa Lushoto hususan Jimbo la Mlalo wameikosea nini hii Serikali hii ya Awamu ya Tano?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shangazi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Soika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye swali la msingi. Maendeleo ni hatua, na tulianza na vijiji vichache na tunazidi kuongeza, na katika awamu ya tatu mzunguko wa pili wa REA vijiji vyote ambavyo vilikuwa havijapata umeme vitapatiwa umeme.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Shangazi kwamba kabla ya mwaka 2022 Disemba vijiji vyote vya kwenye Jimbo lake la Lushoto viitakuwa vimepatiwa umeme kama nilivyotoa majibu kwenye swali la msingi.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana Mheshimiwa Waziri wa Nishati alikuja Musoma, na ninamshukuru kwamba tulienda naye pale kwenye Kata ya Bweli, Mtaa wa Bukoba tukaweza kuwasha umeme, na baada ya hapo tukaenda kwenye mkutano wa hadhara akaahidi kwamba sasa maeneo yote ya Musoma Mjini wataweza kupata umeme kwa gharama ya 27,000.

Hata hivyo, kila wananchi walipojaribu kwenda kulipia wanaambiwa mpaka waraka utoke kwa sababu haujapatikana. Sasa napenda kujua ni lini Mheshimiwa Waziri wa Nishati atatoa waraka ili wale wananchi wangu wa Jimbo la Musoma waweze kupata umeme kwa gharama nafuu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Manyinyi, Mbunge wa Musoma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nakiri kabisa kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yaliyotolewa yanatakiwa kuzingatia na kusimamiwa kama ilivyo na kwa kuwa tumesikia kuna lalamiko la namna hiyo, naomba tulichukue na tutahakikisha kwamba maelekezo ya Mheshimiwa Waziri yanafanyiwa kazi kama ilivyoelekezwa, hakuna kupindisha maelekezo yaliyotolewa.
MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa changamoto ya umeme wa Jimbo la Handeni inafanana kabisa na Jimbo la Arusha Mjini, napenda kuuliza maswali ya nyongeza yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunafahamu kwamba Jiji la Arusha ni jiji la kitalii, lakini bado kuna kata ambazo zinachangamoto kubwa sana ya umeme Kata kama za Telati, Kata ya Olasiti, Olmoti, Moshono, Mulieti kule maeneo ya Losoito, Sokoni 1 na Sinoni. Ningependa kufahamu, je, Wizara ina mpango gani kupitia Mradi wa Peri-urban ili kuhakikisha kwamba wananchi hawa ambao wapo kwenye Jiji la Kimataifa, Jiji la Utalii wanaondokana na changamoto ya umeme katika jimbo letu?

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili….

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa moja tu, hilo ni la nyongeza.

MHE. MRISHO M. GAMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Gambo, Mbunge wa Arusha, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara inapeleka umeme katika maeneo mbalimbali kwa programmes tofauti. Ziko awamu za REA ambazo zimeendelea, ziko programme ya densification, lakini ipo programu peri-urban ambayo inapeleka umeme kwenye maeneo ambayo yana asili ya ukijiji lakini yako mjini. Mkoa wa Arusha tayari umeshanufaika na awamu ya kwanza ya densification, peri-urban kupeleka umeme katika baadhi ya maeneo na iko awamu ya pili ya peri-urban ambayo itakuja, inaanza mwezi wa Saba.

Katika maeneo ambayo hayajapata Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Mwanza na Tanga yatapelekewa umeme katika Mradi huo wa pili wa peri-urban. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba awamu hiyo ya pili ikianza basi na yeye maeneo yake yatapatiwa umeme katika awamu hiyo.
MHE. JUMANNE A. SAGINI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; Jimbo la Butiama lina vitongoji 370, katika awamu zote mbili nilizopita za REA ni vitongoji 147 tu vilipata umeme sawa na asilimia 40. Sasa Naibu Waziri ananihakikishiaje kwamba pia kama njia ya kumwenzi baba wa Taifa, vitongoji 223 vilivyosalia vitapata umeme katika awamu ijayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; sera ya Wizara ni kwamba unapopita umeme taasisi za elimu au afya zilizoko katika maeneo hayo zinapaswa pia kuhakikisha kwamba zinafungiwa umeme, lakini ninazo taarifa katika Jimbo la Butiama zipo shule za sekondari, vituo vya afya na zahanati ambavyo havijapata umeme. Je, Waziri atanihakikishiaje kwamba vituo hivyo vinapata umeme, orodha ninayo ndefu lakini atuhakikishie kwamba TANESCO walioko kule wanaweza wakashusha umeme kabla ya utekelezaji ya awamu ijayo anayosema inayoanza mwezi Julai?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Sagini, Mbunge wa Butiama, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Butiama ni mojawapo ya Wilaya ambayo tayari zimepata umeme katika vijiji vyote vilivyoko na kweli kuna baadhi ya vitongoji ambavyo havijapata umeme. Upelekaji wa umeme kwenye vitongoji ni zoezi endelevu na ni kwa awamu na tunapeleka umeme katika maeneo haya kupitia TANESCO kufanya kazi zao za kila siku lakini pia kupitia katika miradi tuliyokuwa nayo ambayo ilikuwepo densification I, densification IIA, IIB na sasa mwezi wa Saba tutaanza densification IIC ambapo kama tulivyosema tutapeleka vitongoji 648.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vitongoji vyote vilivyoko katika Wilaya ya Butiama, awamu kwa awamu vitapelekewa umeme na vyote vitapatiwa umeme vyote kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali lake la pili, nipende kusema kwamba ni kweli zipo baadhi ya taasisi ambazo zimekuwa zikiachwa bila kupelekewa umeme, lakini wakati wa kuzindua mradi wa REA, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, maelekezo ya Wizara ambayo yalitolewa na Mheshimiwa Waziri wa Nishati, yalisema kwamba katika kupeleka umeme katika awamu hii ya tatu, kisiachwe kijiji au eneo lolote ambalo lina taasisi ya umma ambayo haitapelekewa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, uniruhusu nirudie maelekezo yake kwamba wakandarasi wote wanaopeleka umeme katika awamu ya tatu, mzunguko wa pili, wasiache kupeleka umeme katika taasisi zote za umma ambazo ziko katika maeneo yetu. Vile vile, uniruhusu nisisitize maelekezo mengine mawili ambayo Mheshimiwa Waziri aliyatoa, mojawapo ikiwa ni kwamba watakapokwenda Wakandarasi kupeleka umeme katika maeneo yetu, pamoja na watu wengine na taasisi nyingine watakazoenda, wahakikishe wanapiga hodi kwa Waheshimiwa Wabunge ili Waheshimiwa Wabunge waweze kuwaonyesha maeneo ambayo yana changamoto zikiwa ni pamoja na hizo ambazo ni taasisi zetu za umma.

Mheshimiwa Naibu Spika, agizo la mwisho, alilolitoa ni kwamba ni lazima upelekaji wa umeme ukamilike ndani ya muda ambayo ni kufikia Disemba, 2022.
MHE. FLATEI I. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Jimbo la Butiama ni majimbo ya zamani kama ilivyo Mbulu Vijijini na changamoto ya umeme karibu zinafanana. Zipo Kata za Masieda, Eda Chini, Eshkesh ambazo Mheshimiwa Waziri naye alikuja akaziona. Je, ni lini sasa maeneo hayo niliyoyataja yatapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema awamu ya tatu, mzunguko wa pili wa REA, unapeleka umeme katika vijiji vyote vilivyokuwa vimebakia katika awamu zilizotangulia bila kupelekewa umeme.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mbunge kwamba katika awamu hii inayoanza ambayo pengine imeshaanza kwenye maeneo mengine na kufikia Disemba, 2022 vijiji vyote vilivyo katika eneo lake vitapata umeme na vitongoji vitapata umeme kupitia utaratibu huo huo kwa sababu mkandarasi anapopeleka umeme kwenye Kijiji kimsingi anaunganisha wateja kwenye vitongoji na kuunganisha wateja kwenye kaya na mteja mmoja mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu kwa ujumla kwamba vijiji vyote Tanzania Bara vilivyokuwa havina umeme, vitapelekewa umeme katika awamu ya tatu, mzunguko wa pili wa REA bila kukosa.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itatusaidia kupeleka umeme katika Kata ya Kasokola na Mwamkulu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sebastian, Mbunge wa Mpanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote vilivyokuwa havijapelekewa umeme katika awamu zilizotangulia zitapelekewa umeme katika awamu hii ya tatu, mzunguko wa pili na vijiji kwa kuwa viko kwenye kata, kata hizo pia zitakuwa ni sehemu ya kupata umeme huo ambao Serikali imejipanga vyema kabisa kuhakikisha kwamba umeme unawafikia wananchi katika kipindi cha miezi 18 kuanzia mwezi Aprili.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Matatizo yaliyopo katika Wilaya ya Butiama Mkoa wa Mara yanaonyesha uhalisia wa Wilaya zote ndani ya Mkoa wa Mara kwenye kadhia ya umeme na kwa sababu umeme unaweza kuimarisha usalama na kuweza kukuza uchumi kwa maana kupitia uanzishwaji wa viwanda na vitu vingine. Ningependa kujua ni lini sasa Serikali itahakikisha umeme unapatikana katika wilaya zote ndani ya Mkoa wa Mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, wilaya zote Tanzania Bara zina umeme, maeneo machache katika wilaya hizo ndiyo hayajafikiwa na umeme, kwa hiyo nimhakikishie kwamba maeneo hayo machache ambayo bado hayajafikiwa na umeme kwa maana ya vijiji yatakuwa yamepatiwa umeme katika miezi 18 ijayo. Kama ni umeme wa uhakika kama nilivyotangulia kujibu maswali yaliyotangulia ya msingi, Serikali inaendelea kuwa na jitihada za kuhakikisha inatenga bajeti kuhakikisha inawawezesha TANESCO kuendelea kurekebisha miundombinu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, pia Serikali inatekeleza miradi mikubwa sana ya ufuaji wa umeme Tanzania bara ikiwemo ya Mwalimu Nyerere itakayozalisha megawatt 2,115, Rusumo megawatt 80, Kagati megawatt 14, Ruhudji megawatt 358 na Rumakali megawatt 222. Miradi yote hiyo ikikamilika tutaweka umeme mwingi sana kwenye grid yetu ya Taifa na kuweza kumpatia kila mmoja umeme wa kutosha. Kwa hiyo tunawahakikishieni Wabunge wote kwamba umeme upo na utaendelea kuongezwa, tutarekebisha miundombinu yetu ili kila moja aweze kufikiwa na umeme ili Tanzania ya viwanda iweze kuwa ya kweli.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii ili niulize swali dogo la nyongeza. Katika Jimbo la Manyoni Magharibi ambako mimi natoka kwa maana ya Halmashauri ya Itigi kuna vijiji 15 na vitongoji kadhaa bado havijafikiwa umeme. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri anasemaje juu ya vijiji vyangu ni lini vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Massare, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida ni kati ya mikoa ambayo imejengewa kituo kikubwa kabisa cha kupoza umeme na kipo kingine kinachoongezwa kikubwa pia kwa ajili ya kupitisha umeme kutoka Iringa kupita Singida kwenda Arusha kwa ajili ya kwenda nje ya nchi ambapo ni Arusha kwenda Kenya.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Singida ni mkoa ambao hauna matatizo ya umeme na nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo machache ambayo kwake bado hayajapata umeme, yataendelea kupelekewa umeme kwa kupitia taasisi yetu ya TANESCO, lakini kwa kupitia awamu mbalimbali ikiwemo REA awamu ya tatu, mzunguko wa pili, ambao kwa sasa unaendelea kwa sababu umeme tunao wa kutosha na tunao uwezo wa kupeleka lakini ni kwa awamu kwa awamu kama nilivyotangulia kusema.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Meatu liko nyuma katika utekelezaji wa umeme wa REA, kwa kuwa ni asilimia 46 tu ndiyo iliyotekelezwa. Je, Serikali haioni haja ya kupeleka kwanza kwenye kata saba ambazo hazijafikiwa kabisa ambazo ni Kata ya Mwamalole, Mwamanongu, Mwabuzo, Imalaseko, Kimali na Mbushi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika maswali mengine yaliyotangulia, Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na TANESCO na REA tunapeleka umeme na tumejipanga kupeleka umeme katika maeneo ya vitongoji na vitongoji hivyo ndimo kata zinapopatikana, ndimo vijiji vinapopatikana na wilaya inahudumia maeneo hayo hayo. Kwa hiyo katika awamu ya tatu, mzunguko wa pili, hatujabaguwa nani aanze na nani afuate tutakwenda kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, labda niseme katika awamu hii ya tatu, mzunguko wa pili, tumefanya mambo mawili ya kuhakikisha kwamba tunakuwa na uhakika wa kupeleka umeme katika maeneo yote kwa wakati mmoja. Jambo la kwanza tulilolifanya tumegawa kazi kidogo kwa wakandarasi wachache wachache kuhakikisha kwamba basi mkandarasi anakuwa hana kazi kubwa za kufanya na hivyo kushindwa kumaliza kazi yake kwa wakati katika eneo alilopewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili tulilolifanya, tumehakikisha kwamba tunapeleka wasimamizi katika maeneo hayo ya kanda na kwenye mikoa ambayo yatakuwa yanatokea REA kwenda kuhakikisha kwamba wale wakandarasi tuliowapeleka wanafanya kazi.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Leah kwamba katika kipindi hiki cha REA awamu ya tatu, mzunguko wa pili, ataona matunda makubwa na mafanikio makubwa ya upelekaji wa umeme katika maeneo yote ya vijiji na vitongoji tuliyokuwa nayo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kunipatia niweze kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kata hizi ilikuwa zipatiwe umeme REA awamu ya pili, lakini mpaka tunamaliza REA awamu ya pili kata hizo hazijapatiwa umeme. Je, Serikali inawahakikishiaje watanzania wa Wilaya ya Chemba kwenye kata hizi nilizozitaja, kwamba kwenye awamu hii ya REA awamu ya tatu iliyoanza Machi, 2021 kwamba vijiji hivi na kata zake hazitakwenda kukosa umeme?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili, kumekuwa na changamoto kubwa sana ya ukatikaji wa umeme kwenye maeneo mbalimbali ikiwemo Wilaya ya Chemba na kwenda kusababisha uharibifu wa mali za watumiaji wa umeme. Je, Serikali sasa haioni ni wakati wa kuanza kulipa fidia kutokana na tatizo la ukatikaji wa umeme bila taarifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kunti kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitoe tamko la Serikali kwa niaba ya Serikali, kwamba tunawahakikishia wananchi wote wa Tanzania kwamba vijiji vyote ambavyo vilikuwa havijapata umeme vilivyoko katika kata pamoja na hivyo alivyovitaja Mheshimiwa Mbunge kwamba vitapelekewa umeme katika awamu ya pili ya mzunguko wa tatu wa REA, bila kuacha kijiji hata kimoja. Hiyo ni commitment ya Serikali na tayari mradi umeanza na vijiji vyote vilivyokuwa vimebakia takriban 1,900 vimechukuliwa katika mradi huu na vitapatiwa umeme.

Mheshimiwa naibu Spika, timekuwepo changamoto kadhaa katika awamu zilizotangulia na zile baadhi ya maeneo ambayo yalikuwa yamebaki katika awamu hii ya tatu mzunguko wa pili hakuna hata kimoja kitakachobaki; na hiyo ni commitment ya Serikali. Kwa hiyo Mheshimiwa namuhakikishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimshukuru Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Chemba Mheshimiwa Monni amekuwa naye mstari wa mbele katika kufuatilia umeme wa wananchi wake; na sisi kama Wizara na Serikali tutahakikisha kwamba tunapeleka umeme katika mazingira hayo kwa kushirikiana na Wabunge wa maeneo yote. Ndio maana sasa swali lililoulizwa limejibiwa lakini pia na wengine wanaendelea kufuatilia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika swali la pili alizungumiza kuhusu kukatika kwa umeme na nizungumzie katika eneo la Chemba. Yapo matatizo ambayo yanapelekea umeme kukatika; na kwa eneo la Dodoma tunalo tatizo moja kubwa sana. Udongo wa Mkoa wetu wa Dodoma ni udongo tepetepe inaponyesha mvua, kwa hiyo nguzo zimekuwa zikianguka na kulala panapokuwa panatokea hali ya hewa yenye mvua nyingi na udongo kuwa tepetepe. Na katika kulitatua hilo tumehakikisha basi tumeanza kuweka vitu vinavyoitwa concrete poles ambazo ni nguzo za zege zinaweza kwenda chini zaidi na zitahimili mzingo kwa sehemu kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwa Jimbo la Chemba umeme unaokwenda Chemba unaenda katika sub-station yetu ya Babati unapita Kondoa, unakwenda Chemba, unakwenda Kiteto, unakwenda mpaka Kilindi, kwa hiyo ni parefu sana. Kwa Mkoa wa Dodoma imeamuriwa kwamba zijengwe sub-station nne zinazoitwa ring circuit ambazo zitakuwa zikiuzunguka mji wa Dodoma na zitapunguza mahitaji ya umeme kwenye msururu mrefu. Kwa mfano kutoka Kondoa kwenda Chemba kuna kilometa kama 30. Sasa ile Kiteto na Kilindi zitaondolewa kwenye mstari huu ili umeme unaokwenda Chemba uwe wa uhakika na uuhudimie wale wananchi walioko pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini tumekuwa tukiwaelekeza wenzetu waendelee kutoa taarifa kwa wananchi wao ili waweze kupata taarifa kwamba umeme utakatika na wajiandae kwa mazingira kama hayo.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, miaka miwili iliyopita Waziri wa Nishati alitembelea Kituo cha Afya cha Makorongo na kwa sababu ya umuhimu wa Kituo kile cha Afya alielekeza umeme uwekwe. Kituo kile kinahudumia Kata tano lakini mpaka leo hii kituo kile hakijapata umeme. Naomba sasa kujua, ni lini Wizara itatekeleza agizo lile la Waziri wa Nishati na Madini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni, Mbunge Chemba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Waziri yalitakiwa yatekelezwe na kwa vyovyote vile yatakuwa katika hatua za utekelezaji kwa sababu uunganishaji wa umeme siyo jambo la siku moja. Naomba tulichukue na tukalifanyie kazi na kuhakikisha katika muda mfupi umeme unawashwa katika Kituo hicho cha Afya kwa ajili ya kuhudumia wananchi.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata 29 za Wilaya ya Mbozi, Kata tatu za Bara, Kilimpindi na Nyimbili bado hazijapelekewa umeme. Naomba kufahamu ni lini Serikali itapeleka umeme katika kata hizo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shonza kuhusu kupeleka umeme katika kata alizozitaja katika Jimbo la Mbozi. Katika Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili wa REA iliyoanza Machi tutahakikisha tunapeleka umeme maeneo yote ambayo yalikuwa hayajapata umeme. Hivyo na yeye atakuwa mmojawapo kati ya wale watakaopata umeme katika awamu hii.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Tunduru Kusini lina matatizo makubwa sana ya umeme hasa vijiji vyake zaidi ya asilimia 70 bado havijapata umeme. Je, ni lini Mradi wa REA Awamu ya Tatu B utaanza katika Jimbo la Tunduru Kusini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Tunduru kwa kusema ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili inazo jumla ya Lot 37 za kupelekeza umeme katika maeneo yetu ya vijiji. Katika hizo Lot 37, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kwamba tayari maeneo yote yaliyotakiwa kupelekewa umeme ambayo hayakuwa na umeme yamechukuliwa katika hizo Lot 37 na tayari tumeshazindua kuanzia Machi 15, pale Manonga na tunaendelea kuwatuma wakandarasi kuripoti katika maeneo yetu husika.

Mheshimiwa Natibu Spika, nikumbushie tu, agizo ambalo tumeshalitoa kwamba wakandarasi wote wanaenda kupeleka umeme katika maeneo hayo pamoja na maeneo mengine watakayopiga ripoti. Wapige ripoti kwa Waheshimiwa Wabunge ili kuwaonesha maeneo ambayo yanahitaji umeme kwa haraka na kwa ufasaha zaidi ili kuweza kushirikiana kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivyo, itapunguza yale maswali ambayo tunaulizwa kwa sababu Waheshimiwa Wabunge watakuwa wamepata uhakika kwamba katika eneo lake mkandarasi anafika. Kwa hiyo, niwasisitize wakandarasi wafike katika maeneo ya Waheshimiwa Wabunge na kutoa taarifa ili Waheshimiwa Wabunge wapate hiyo taarifa na sasa kazi iweze kuendelea vizuri.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa umeme unaozalishwa katika Sub-station ya Mbagala ni chini ya asilimia 20 tu unaotumika Mbagala na asilimia zaidi ya 80 unaenda kutumika Mkuranga. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga sub-station kule Mkuranga ili kuwapoza watu wa Mbagala waendelee kutumia umeme wao?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa Jimbo la Mbagala ndiyo Jimbo ambalo lina watumiaji wengi wa umeme ukilinganisha na mikoa mingine ya Ki-TANESCO, je, Serikali ina mpango gani wa kulifanya Jimbo la Mbagala kuwa mkoa wa Ki-TANESCO?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chaurembo, Mbunge wa Mbagala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Mbagala tunayo Sub- station inayozalisha Megawatts 48 na Megawatts 40 zinakwenda Mkuranga kama alivyosema kwa sababu kuna viwanda vingi sana pale zinabaki Megawatts 8 tu. Tunapata umeme wa Mbagala kutoka Ubungo kupitia Gongolamboto lakini tunapata umeme mwingine kutoka Kurasini. Pale Kurasini tunapata Megawatts kama 26 hivi, zinazoenda kujazia pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba umeme unapungua katika eneo la Mbagala kwa sababu mahitaji yamekuwa makubwa. Hata hivyo, kama tulivyosema kwenye swali la msingi, tunaongeza uwezo wa kituo hicho cha Mbagala kwa kuweka MVA 50 lakini pia cha Kinyerezi ambacho pia kitaleta umeme pale Mbagala.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali hilohilo ni kwamba tayari Serikali inafanya feasibility study ya kujenga sub-station nyingine kumi na kuziboresha nyingine kadhaa katika maeneo yetu ya Tanzania. Mkuranga kwa sababu ya umuhimu wake wa kuwa na viwanda vingi sana ni eneo mojawapo ambalo litapelekewa sub-station katika siku za hivi karibuni ili kupunguza mzigo mkubwa ambao vituo vyetu vya Mbagala na Kinyerezi vinaupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, Mkoa wa Dar es Salaam mpaka sasa unayo mikoa ya ki-TANESCO minne na hivi karibuni yamekuja maombi ya Kigamboni kuwa ni Mkoa wa ki-TANESCO na bado yanafanyiwa kazi. Niombe kwamba kwa kuwa Mheshimiwa Mbunge amelisema, tutaenda kuangalia vigezo kwa sababu kuna kuangalia idadi ya wateja, makusanyo, line ya umeme mkubwa na mdogo katika eneo husika, vigezo vikikidhi basi, mamlaka husika zitaamua na huduma zitapelekwa karibu zaidi na wananchi.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Spika, ahsante pamoja na majibu ya mazuri ya Serikali ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto ya miradi kutokukamilika kwa wakati. Nini kauli ya Serikali kwa wakandarasi ambao hawamalizi miradi yao kwa wakati na kuchelewesha huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili kumekuwa na wimbi kubwa sana la wizi wa miundombinu ya umeme, mfano kule Moshi Manispaa, katika Kata za Soweto, Boma Ng’ombe, Barabara ya Bonite pamekuwa na wimbi la vijana ambao wanaiba miundombinu hii. Je, Serikali hii inachukua hatua gani kudhibiti uharibifu huu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kauli ya Serikali kuhusiana na miradi ambayo haijakamilika ni kwamba, kwanza ifikapo Disemba mwaka huu 2021 miradi yote ambayo siyo ya REA III round II itakuwa imekamilika kwa maana ya REA II na REA III round I itakuwa imekamilika.

Mheshimiwa Spika, tulikuwa na changamoto kidogo zilizopelekea miradi hii kuchelewa, sababu mojawapo ikiwa ni kwamba ni vile vifaa ambavyo vilikuwa vinaagizwa nje ya nchi vilichelewa kufika kwa sababu ya lockdown za wenzetu kule kushindwa kuleta vile vifaa kwa wakati. Shida nyingine ilikuwa ni maeneo mengine miundombinu kuharibiwa na mvua kali na hivyo watu wakashindwa kukamilisha kazi zao kwa wakati. Hata hivyo, tumejiwekea utaratibu na tunawaahidi Watanzania kwamba ifikapo Disemba mwaka huu hakutakuwa kuna mradi wowote wa REA III round I au REA II ambayo inaendelea, itakuwa yote imekwisha. Miradi ambayo itakayokuwa inaendelea ni ya REA III round II ambayo nayo Disemba mwakani itakamilika.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha mambo haya hayajitokezi tena, Serikali ilielekeza kwamba vifaa vyote vipatikane hapa nchini na kweli vinapatikana. Hiyo inatuongezea speed ya kufanya kazi hizi na kuzimaliza mapema.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo Serikali imelifanya ni kuhakikisha sasa inatoka kwenye kufanya kazi hizi kwa mtindo wa goods na kuziweka kwenye works, kwamba mtu atalipwa baada kukamilisha kipande fulani cha kazi ambacho anatakiwa kukifanya na hiyo inatusaidia kusimamia vizuri maeneo haya.

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo Serikali imelifanya, tumehakikisha sasa tunakwenda kila kanda na kila mkoa kuweka msimamizi wa miradi yetu ya REA, akae kule masaa 24 akimsimamia mkandarasi anayefanya kazi kuhakikisha kwamba kazi inakwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, jambo la nne, tumehakikisha kwamba, wale wakandarasi wanaokwenda kwenye maeneo yetu tumewakabidhi kwa Waheshimiwa Wabunge ili na wenyewe wawe wasimamizi namba moja wa kuhakikisha kila siku wanawaona site na pale ambapo panatokea hitilafu ya kuwa mzembe mzembe, basi taarifa hizo zinatufikia mara moja. Tunaamini njia hizo zitatusaidia.

Mheshimiwa Spika kwenye jambo la pili; jambo la wizi siyo la mtu mmoja kulikemea, tunawaomba wenzetu tuendelee kushirikiana, sisi kama Wizara tunawapa support kubwa sana wakandarasi wanapotoa taarifa za kuibiwa, tunasaidiana nao moja kwa moja kuhakikisha kwamba tunafuatilia, kuhakikisha tunawachukulia hatua wale walioiba miundombinu. Pia tunaweka mikakati mingine ya ziada ya kuwasaidia wale wakandarasi kuweka vifaa vyao katika godown za TANESCO ili angalau viwe katika usalama zaidi.

Mheshimiwa Spika, vile vile tumewaelekeza, wao ndiyo wenye wajibu wa kuhakikisha mali hizo haziibiwi ili wafikishe mizigo ile na kazi ifanyike kwa wakati. Tunaamini kufikia Disemba mwakani, jambo la kupeleka umeme REA III round II litakamilika kwa muda uliopangwa kwa mujibu maelekezo ya Serikali. Nashukuru.
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Moja ya changamoto inayosababisha Tunduru kukatika umeme mara kwa mara ni ubovu wa miundombinu ya kutoka Namtumbo kuja Tunduru na kutoka Tunduru kwenda Nanyumbu mpaka Masasi.

Je, Serikali haioni sasa ni muhimu kuweka nguzo za zege kutoka Namtumbo mpaka Tunduru na kutoka Tunduru mpaka Masasi ili kudhibiti uharibifu wa nguzo za umeme unaotokea mara kwa mara na kufanya umeme kukatika katika maeneo hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Daimu na muuliza swali mwenyewe Mheshimiwa Hassan, kwa nia ya kuendelea kuhakikisha kwamba miundombinu inaendelea kuboreshwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Mkoa wa Ruvuma kwa mwaka huu wa fedha umetengewa shilingi 1,200,000,000 kwa ajili ya marekebisho ya miundombinu mbalimbali ya umeme ikiwemo nguzo, transfoma na waya. Lakini kabla sijasema kuhusiana na uwepo wa nguzo za zege kwanza niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote watusaidie katika kuhakikisha miundombinu yetu ya umeme inalindwa kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko huko Tunduru jana kuamkia leo na upo Mwenge, lakini wananchi wamechoma miundombinu ya umeme na kusababisha umeme kukatika katika maeneo hayo. Na ni kweli kwamba tunatoka kwenye nguzo za miti kwenda kwenye nguzo za zege kwenye maeneo yenye matatizo korofi. Maeneo ambayo kuna wadudu waharibifu kama mchwa, maeneo ambayo ni oevu yana majimaji, lakini pia kwenye maeneo ambayo ni ya kwenye hifadhi ambako hakuwezi kufikika mara kwa mara na wanyama waharibifu wanakuwa wanaiharibu ile miti yetu ya kushikilia umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye maeneo ambayo hayana matatizo hayo tunawaomba Waheshimiwa Wabunge, waendelee kuwa mstari wa mbele kuhamasisha ulinzi wa miundombinu yetu ili isiharibiwe.

Kwa hiyo, nimuhakikishie Mheshimiwa Daimu kwamba maeneo ambayo nimeyataja yanayohitaji nguzo za zege yatapelekewa nguzo za zege na tayari tumeshaanza. Wazabuni wanaotengeneza nguzo za zege tumeshawapata na kwenye baadhi ya maeneo kama mnavyoona Waheshimiwa Wabunge, tayari tumeshazipeleka na tutahakikisha miundombinu inaboreshwa zaidi. (Makofi)
MHE. SAMWELI H. XADAY: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kwa kuwa kwa sasa Serikali haina utaratibu wa kufuata mipaka ya kiutawala katika kutoa huduma za umeme, kwa mfano, Kata ya Masakta iko kwenye Wilaya ya Hanang kiutawala lakini inahudumiwa na TANESCO Babati na hii imekuwa ikisababisha usumbufu kwa wananchi kufuatilia huduma. Je, Serikali ina mkakati gani kurekebisha tatizo hilo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Serikali imefanya kazi kubwa kwenye mradi wa REA kupeleka umeme vijijini lakini kwenye vijiji husika maeneo yanayofikiwa au watu wanaopata umeme ni wachache. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba wananchi wengi zaidi wanapata umeme na kufika kwenye hatua ya vitongoji hasa kwenye Jimbo langu la Hanang? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Samweli Xaday, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya maeneo ambapo mikoa au wilaya za ki-TANESCO haziendani na mikoa au wilaya za kiserikali na nia kuu ya Shirika la TANESCO chini ya Serikali ilikuwa ni kuhakikisha kwamba huduma zinawafikia wananchi katika maeneo ambayo yanafikika kirahisi. Kwa kutoa mfano katika Mkoa wa Manyara, Wilaya ya Kiteto inahudumiwa na Mkoa wa Dodoma lakini tunayo wilaya ya ki-TANESCO inaitwa Simanjiro na wilaya nyingine inaitwa Mererani. Wilaya ya Simanjro ki- TANESCO inahudumiwa na Mkoa wa Kilimanjaro lakini wilaya ya ki-TANESCO ya Mererani inahudumiwa na Arusha.

Mheshimiwa Spika, kwa wanaofahamu ni rahisi sana kutoka Simanjiro kwenda Kilimanjaro, ni rahisi sana kutoka Mererani kwenda Arusha kuliko kurudi Makao Makuu ya Mkoa wa Manyara ambapo ni Babati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nia ya Serikali ilikuwa ni kuhakikisha kwamba huduma zinawafikia wananchi kirahisi wanapohitaji kwenda ofisini kupata huduma lakini pale ambapo TANESCO inatakiwa iende kuwafuata wananchi kuwahudumia au kwenda kufuata vifaa katika bohari.

Mheshimiwa Spika, Serikali imepiga hatua kubwa sana ya kuhakikisha miundombinu inafika karibia kila sehemu na hivyo ni rahisi sana kufikisha huduma kwa wananchi mbalimbali kwenye maeneo hayo. Kwa hiyo, kila inapowezekana Serikali imeamua sasa ipeleke utawala wa ki-TANESCO sawasawa na utawala wa kiserikali ili kuhakikisha mtu anapata huduma kutoka kule ambako anategemea kuipata na maendeleo hayo ataendelea kuyaona kadri muda unavyozidi kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili ni kweli na kama tunavyofahamu maendeleo ni hatua. Kwa harakaharaka tu mwaka 2007 wakati REA inaanza ilipita vijiji 506 ndio vilikuwa na umeme lakini taarifa zinaonyesha kufikia 2015 tulikuwa tuna vijiji 2018 vyenye umeme na kufikia mwaka huu 2021 taarifa zetu zinaonyesha tuna vijiji 1950 kati ya 12,268 ambavyo viko Tanzania kwa ujumla wake. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba maendeleo ya kupeleka umeme ni endelevu na kadri Serikali inavyoendelea kupata pesa kwa kujibana na kwa kujihamasisha yenyewe inaendelea kuepeleka huduma hii na tutahakikisha inamfikia kila mwananchi anayehitaji kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nataka kujua ni lini Serikali italipa fedha hizo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa sababu mradi huu umekaa sasa ni miaka minne, je, Serikali ipo tayari kuwapa kifuta jasho wananchi ambao wamesubiri kwa muda wote huo wakati wakisubiri malipo haya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Bonnah, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nieleze kidogo kwamba fidia inayotakiwa kufanyika katika maeneo haya ni fidia ambayo ni ya miradi ambayo tunaweza kuiita miradi ambatanishi. Kimsingi umeme unaozalishwa katika Bwawa letu la Mwalimu Nyerere megawatt 2,115 unatakiwa utoke Mwalimu Nyerere kuja kuingia katika Gridi ya Taifa na unaingilia kwenye Gridi ya Taifa pale Chalinze. Kwa hiyo, itajengwa hiyo njia ya kutoka Mwalimu Nyerere kuja Chalinze, lakini Chalinze kwenda Kinyerezi na Chalinze kuja Dodoma.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kuhusu exactly fidia italipwa lini ni tusema ni kabla ya kufika mwezi wa kumi mwaka huu, kwa sababu lazima kwanza tulipe fidia ndiyo tutaweza kujenga njia hiyo ya kupeleka umeme. Njia hiyo ya kupeleka umeme lazima ikamilike kabla ya tarehe 14 Juni, 2022 ili iweze kusafirisha ule umeme utakaozalishwa pale Mwalimu Nyerere. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba fidia itatolewa kwa wakati na haitochelewa kwa sababu kuchelewa kwa fidia hiyo kutasababisha mradi wa Mwalimu Nyerere usiweze kuingiza umeme wake kwenye grid.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili kama Serikali ipo tayari kuwapa kifuta jasho, niwahakikishie waheshimiwa Wabunge wote kwamba Serikali ya Chama cha Mapinduzi inayoendeshwa na Mama yetu Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan ni Serikali sikivu na isiyoonea mwananchi taratibu za fidia zipo na zinafahamika kwamba inalipwa kwa namna gani na ndani ya wakati gani. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwa fidia stahiki italipwa kwa kila anayestahili kulipwa kwa mujibu wa viwango vya kisheria vilivyowekwa na muda uliowekwa kwa ajili ya hesabu hizo.
MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu yanayotia matumaini kutoka Serikalini, lakini ametaja vijiji ambavyo bado havijapata umeme, kuna kimoja hakukisema ambacho kinaitwa Ruhoko. Kijiji hiki kimefungwa waya zote, kimefungwa transfoma, kimewekwa nguzo, kila kitu kimekamilika mwaka wa pili leo umeme haujawashwa kwa nini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; amesema vijiji nane kati ya vijiji 94 ambavyo vimesalia kupata umeme, lakini na vitongoji 515, kati ya vitongoji hivyo vyenye umeme ni 86 tu zaidi ya vijiji 400 havina umeme. Utaratibu ukoje kuhusu vitongoji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Samson Jasson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, na-declare interest kwamba mimi natoka Jimbo la Bukoba Mjini na kabla ya utumishi wa Bunge nilikuwa mtumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Bukoba. Kijiji cha Luoko nakifahamu kiko katika Kata ya Katoro na katika ufuatiliaji wetu Kijiji cha Luoko tayari kilishapelekewa umeme, lakini tulipata changamoto ya kutopata wateja wa kuwaunganishia umeme katika kijiji hicho na hivyo miundombinu ile ilikuwa haijaanza kufanya kazi.

Waheshimiwa Wabunge, watakumbuka kuna kipindi Mheshimiwa Waziri wa Nishati alisema kwamba, wale ambao atawapelekea umeme na hawatataka kuunganisha basi itabidi tutumie jitihada za ziada za kuwalazimisha kuunganisha ule umeme. Ningekuwa naweza kufanya hivyo na Kijiji cha Luoko kingekuwa kimojawapo ambapo tungewalazimisha wananchi kuunganisha umeme huo.

Mheshimiwa Spika, lakini tayari tumeshafanya sensitization na wananchi wa Luoko wako tayari kuunganishiwa umeme. Tumemuelekeza mkandarasi aliyekuwa anapeleka umeme katika kijiji hicho anaitwa Nakroi ambaye alipeleka umeme katika Awamu ya Pili ya Mzunguko wa REA na yuko tayari kupeleka umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Kijiji cha Luoko kitapepekewa umeme ndani ya muda mfupi baada ya utaratibu wa kuunganishiwa wananchi kuwa umekamilika.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili kuhusiana na vitongoji vya Jimbo la Bukoba Vijijini; upelekaji wa umeme kwenye vitongoji ni zoezi endelevu na kama ambavyo nimekuwa nikisema, tunapeleka umeme kwenye vitongoji katika njia tatu; kwanza TANESCO wamekuwa wakiendelea kupeleka umeme katika maeneo ya vitongoji vyetu, lakini njia ya pili ni kupitia hiyo miradi ya REA ambayo tumekuwa tukipeleka umeme kwenye vijiji na tunapeleka kwenye vitongoji, lakini njia ya tatu uko mradi maalum wa kupeleka umeme kwenye vitongoji unaoitwa densification. Na tulianza na Densification Awamu ya Kwanza tulipeleka katika mikoa nane, tukaja na Densification Two (A) tukapeleka katika mikoa tisa na sasa tuko Densification Two (B) inaendelea katika mikoa kumi na tutamalizia na Densification Two (C) ambayo tunatarajia ianze mwezi Julai kupeleka katika mikoa inayobakia.

Mheshimiwa Spika, tukiri kwamba hatuwezi kupeleka katika vitongoji vyote kwa wakati mmoja, lakini kama tunavyosema upatikanaji wa fedha na upelekaji wa umeme ni zoezi endelevu tunaamini ifikapo 2022 vijiji vyote Disemba vitakuwa vina umeme na kwenye vitongoji tutaendelea kupeleka kwa kadiri ya kuhakikisha kwamba, kila mwananchi anafikiwa na huduma ya umeme. Serikali Sikivu inapeleka umeme kw wananchi kwa maendeleo yao wenyewe.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa ni ahadi ya Chama Tawala na vilevile ahadi ambayo ipo kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwamba mapema mwaka huu wa fedha vijiji hivyo vitakuwa vimekamilishiwa kupata umeme.

Je, ni lini sasa Serikali itakamilisha kupeleka umeme kwenye vijiji vilivyobaki vya Mkoa wa Tanga hasa Vijiji vya Lushoto na Kilindi ambako kuna hali ngumu zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwa na tatizo kubwa la kukatika kwa umeme kwenye Vijiji vya Handeni, Kilindi na Lushoto linalosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha. Je, ni lini Serikali sasa itamaliza tatizo hilo kwa kubadilisha miundombinu ya umeme hasa katika maeneo ya njia ya umeme kutoka Mombo kwenda Lushoto? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Husna Sekiboko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni commitment ya Serikali kuhakikisha kwamba vijiji vyote 1,974 ambavyo mpaka sasa havijapata miundombinu ya umeme, vitapata kufikia Desemba, 2022. Hii awamu ya tatu mzunguko wa pili wa REA utahakikisha kwamba unamaliza maeneo yote ambayo yalikuwa hayajapata umeme na hivyo kufikisha umeme katika vijiji vyote 12,268 ambavyo vilikuwa bado havijapata umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, yeye na Waheshimiwa wengine wote kwamba ifikapo Desemba mwakani tutakuwa tumefikisha umeme katika vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili, kwanza napenda kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote wa Mkoa wa Tanga kwa ufuatiliaji mzuri kabisa wa miundombinu ya umeme katika mkoa wao. Mojawapo ya maeneo ambayo yalikuwa yana matatizo makubwa ya umeme ni Tanga. Serikali kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO tumehakikisha tunamaliza tatizo la umeme katika Mkoa wa Tanga.

Mheshimiwa Naibu Spika, uniruhusu niseme tu kidogo kwamba Tanga ina matumizi ya umeme takribani Megawatts 110 na wanapata umeme katika vyanzo viwili pale Hale Megawatts nne na New Pangani Megawatts 68 na umeme mwingine pia unatoka kwenye kituo chetu cha Chalinze kwenda Tanga. Sasa hizo njia zinakuwa ni ndefu kidogo na hivyo umeme mwingine unapotea njiani.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile, kutoka Chalinze kwenda Tanga, ile njia iliyojengwa pale inashindwa kubeba umeme mkubwa, kwa hiyo, tumeamua kuweka mkakati wa muda mrefu wa kujenga njia ambayo itakuwa ni ya Kilovolt 220 itakayoweza kubeba umeme mkubwa kwa ajili ya kufikisha Tanga bila kukatika. Kwa hiyo, tunajiandaa, tumeshafanya feasibility study, tumeshapata maeneo ya kujenga sub-station ikiwepo eneo la Segera, tutamaliza tatizo hilo. Kwa sasa, Timu yetu ya TANESCO kupitia Shirika lake la ETDCO iko kazini inaendelea kurekebisha miundombinu ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, tulipata takribani shilingi bilioni 4,500 kurekebisha miundombinu ya umeme ya Tanga ikiwemo kurekebisha nguzo, waya na vikombe kwa kilometa zaidi 2,000 na maelekezo ya Wizara ni kwamba ifikapo Mei, 2021 iwe imekamilika. Hivyo timu yao TANESCO kupitia ETDCO ni kubwa na inaendelea kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo, tunawahakikishia wananchi wa Tanga kupitia Wabunge wao kwamba kilio chao tunakifanyika kazi. Vile vile maeneo mengine tutaendelea kuhakikisha tunarekebisha miundombinu ili kuondoa matatizo yaliyopo. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza. Halmashauri ya Wilaya ya Liwale ina vijiji 76, vijiji 34 bado havijapatiwa umeme. Naona uzalishaji wa vijiji vifuatavyo mahitaji ya umeme ni makubwa sana; Kijiji cha Mlembwe, Lilombe, Kikulyungu, Mkutano, Mpigamiti, Ngorongopa, Ngongowele, Kimambi, Nahoro na Ndapata, vijiji hivi kwa sababu ya uzalishaji wake mahitaji ya umeme ni makubwa sana. Je, Serikali ni lini mtatupelekea umeme kwenye vijiji hivi ili kuwatia wananchi hamasa zaidi waweze kuzalisha zaidi mazao ya chakula na biashara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza pia Mheshimiwa Kuchauka kwa sababu yeye ni mmojawapo wa Wabunge wanaofuatilia pia maendeleo ya majimbo yao katika maeneo mbalimbali katika likiwepo eneo la umeme. Kama nilivyosema hapo mwanzo ni kwamba vijiji vyote ambavyo havijapata umeme, kufikia Desemba, 2022 vitakuwa vimepatiwa umeme vikiwepo vijiji vyote alivyovitaja vya Jimbo la Liwale. Tunaomba aendelee kutusaidia na kusimamia utekelezaji ambao utafanyika katika maeneo yake.
MHE. DKT. ALFRED J. KIMEA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona nami niulize swali dogo la nyongeza. Napenda kuipongeza Serikali kwani ndani ya Kata zangu zote 11 kwenye Jimbo la Korogwe Mjini umeme umefika, lakini changamoto ni kwamba ndani ya Kata hizo ipo Mitaa mingi ambayo umeme haujafika kabisa. Je, Serikali inawaahidi nini wananchi wa Korogwe katika kutatua changamoto hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kimea, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, TANESCO inapeleka umeme katika maeneo mbalimbali kwa program za kila siku za kawaida, kwenye Mitaa, Vijiji na Vitongoji. Pia zipo program nyingine ambazo zinapeleka umeme kwenye Mitaa na Vijiji vyetu ikiwemo REA yenyewe, densification na peri-urban.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa Mheshimiwa Dkt. Alfred ambapo tayari Kata zake zote na vijiji vyake vyote vina umeme, yale maeneo machache ambayo hayana umeme, mradi wetu wa densification utapelekea umeme katika maeneo hayo kuanzia mwezi Saba. Pia tunavyo Vitongoji na Mitaa takribani kama 3,000 ambavyo vitapelekewa umeme, kwa hiyo, Vitongoji vyake na Mitaa yake Mheshimiwa Mbunge pia ni sehemu ya maeneo hayo yatakayopelekewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, pale ambao densification tu itaanza mwezi wa Saba, Mheshimiwa ataweza kupata umeme katika eneo lake kwa sababu amekuwa akifuatilia sana ofisini kwetu na ni mfuataliaji mzuri wa maendeleo ya wananchi. Kwa hiyo, nawapongeza wananchi kwa kupata Mbunge mfuatiliaji kama wa aina yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Kwa kuwa Kitongoji cha Banawanu katika Kata ya Mseke kiko karibu sana na Mji wa Iringa Mjini na kipo katikati ya Tosamaganga pamoja na Uwachani; na hii ilikuwa ni ahadi ya Mbunge ambaye ndiye mimi kwamba tutawapelekea umeme. Je, ni lini sasa TANESCO itapeleka umeme ili hata kunifichia aibu Mbunge mwenzake?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Kiswaga kwa kutoa ahadi za ukweli kwa wananchi wake kuwaahidi kuwapelekea umeme. Nawaahidi Waheshimiwa Wabunge wote walioahidi kupeleka umeme kwa wananchi wao kwamba ahadi hizo zilikuwa ni za ukweli na Serikali sikivu inayoongozwa na Mheshimiwa Rais, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan itatekeleza.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kitongoji alichokisema kama nilivyosema, mradi wetu wa densification ambao sasa tupo IIB utapeleka katika Vitongoji ambavyo vilikuwa havijapata umeme, lakini maeneo mengine ambayo hayajapata umeme kwa sasa kwa maana ya vijiji, vitongoji vilivyomo, tulivyovitaja 1,474 vitapata umeme pia katika awamu hizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa wananchi kwamba umeme utapelekwa na ahadi ya Mheshimiwa Jackson Kiswaga itakuwa ni ya ukweli kuanzia mwezi Julai.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu ya Serikali. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kuongeza vijiji tisa ambavyo viliachwa katika mzunguko wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika Mzunguko wa Pili wa REA Awamu ya Tatu, Serikali imetenga wigo mdogo wa kusambaza umeme katika vijiji ambao ni kilometa moja.

Je, Serikali haioni namna ya kuongeza wigo kutokana na mtawanyiko wa jinsi vijiji vyetu vilivyo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kukatika katika kwa umeme katika Jimbo la Meatu na Mkoa wa Simiyu kwa ujumla kumeathiri utekelezaji wa shughuli za maendeleo za wananchi: Je, ni lini kituo cha kupoozea umeme kitakamilika katika Mkoa wa Simiyu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba katika upelekaji wa umeme kwenye maeneo yetu hatuwezi kufika katika maeneo yote kwa wakati mmoja. Ni kweli kwamba wigo uliopo hautoshelezi mahitaji tuliyokuwa nayo kwa sababu mahitaji ni makubwa kuzidi uwezo tuliokuwa nao.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwamba mara kwa mara tumekuwa tukiongeza wigo kwa maana ya kupanua scope ya kazi ambayo tunakuwa tumempa mkandarasi kulingana na mahitaji ya eneo husika.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Leah, ambaye amekuwa mfuatiliaji mzuri sana wa masuala ya umeme ya Jimbo lake, kwamba tutakapokwenda katika utekelezaji, tutaongeza wigo kama ambavyo tayari tumeongeza wigo wa vijiji tisa ambavyo Mheshimiwa Waziri amevitaja hapo kuhakikisha kwamba tunawafikia wananchi wote kuwapelekea umeme.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili; ni kweli Mkoa wa Simiyu unapokea umeme kutoka maeneo matatu; Mwanza, Shinyanga (Ibadakuli) na Bunda. Umeme huo unakuwa siyo wa uhakika kwa sababu unasafiri umbali mrefu. Hivyo Serikali imechukuwa jitihada za kuamua kujenga kituo cha kupooza umeme pale Imalilo katika Mkoa wa Simiyu ambacho kitagharimu takribani shilingi bilioni 75 na ujenzi wa transmission line ya kilometa 109 kutoka Ibadakuli (Shinyanga) mpaka pale Imalilo.

Mheshimiwa Spika, kituo hiki tayari kilizinduliwa na Mheshimiwa Waziri. Ujenzi wake ulizinduliwa tarehe 3 Machi, kwa kuweka jiwe la msingi na tunatarajia kwamba mwezi Julai tutakuwa tayari tumekamilisha taratibu za manunuzi na kufikia mwishoni mwa mwaka ujao Desemba, kituo hicho kitakuwa kimekamilika chenye kuweza kusafirisha msongo wa kilovoti 220.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mkoa wa Simiyu utakuwa una uhakika wa umeme kwa sababu umeme mkubwa utakuwa unapoozwa pale na kusambazwa katika maeneo yote ya Mkoa wa Simiyu na hivyo tatizo la kukatika katika kwa umeme litakwisha. (Makofi)
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Moja, baada ya ufuatiliaji wa karibu sana kwenye suala hili imedhihirika wazi kwamba kwa Jimbo la Njombe ni vijiji vinne tu, Mgala, Ngalanga, Mtila na Mbega ndivyo vilivyoingizwa kwenye Mpango ambao Mheshimiwa Naibu Waziri anauongelea. Kuna vijiji takriban 20 ambavyo vimesahaulika, vijiji hivyo ni Hungilo, Uliwa, Utengule, Diani, Makolo, Lugenge, Mpeto n.k. Naomba Serikali itoe kauli kuhusiana na suala hili na iwadhihirishie wananchi wa Njombe kama sasa baada ya maongezi kati yangu, Waziri na REA vijiji vilivyobaki vyote vimeingizwa katika Mpango huo.

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Pamoja na vijiji vingi kuunganishwa na hasa kwenye Jimbo letu la Njombe Mjini bado tuna ukatikaji wa umeme mkubwa sana ambao unaashiria kwamba pamoja na kuunganishwa, tatizo hili litaendelea kuwa kubwa. Tunaomba maelezo ya Wizara kuhusiana na ukatikaji wa umeme katika Mji wa Njombe ambao ni endelevu na hauishi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ni kweli mara ya kwanza vilichukuliwa vijiji vinne lakini baada ya Mheshimiwa Mwanyika kuwasiliana na ofisi na tunamshukuru na kumpongeza kwa ufuatiliaji wake mkubwa, Wizara imeamua iongeze scope ya kazi ya awali na kuongeza vijiji hivyo.

Mheshimiwa Spika, kimsingi vilikuwa havikuachwa lakini vilikuwa vimebaki kwasababu viko katika eneo linalokaribiana na mji. Kwa hiyo, vilikuwa havikuingia kwenye mradi wa REA lakini tumevichukua tukivi-treat kama peri- urban area. Kwa hiyo, vijiji hivyo 20, nimhakikishie Mheshimiwa Deo Mwanyika kwamba vimeingia na vitafanyiwa kazi katika awamu hii ya kupeleka umeme vijijini.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, ni kweli. Maeneo ya Njombe yana tatizo kubwa sana la ukatikaji wa umeme. Naomba nitumie muda kidogo tu kukueleza tatizo kubwa tulilokuwa nalo Njombe na hatua taunazozichukua. Njombe inapata umeme kutoka katika kituo chetu cha kupooza umeme cha Makambako na kuna kilometa 60 kutoka pale Makambako mpaka Njombe, Njombe Mji na eneo kubwa la Mkoa. Sasa Njombe tunayo matatizo makubwa matatu.

Mheshimiwa Spika, tatizo kubwa la kwanza ni baraka ambazo Njombe imezipata ya kuwa na miti mingi sana. Ile miti, pamoja na sisi kufyeka ile line ya kupitisha umeme, lakini miti inayokuwa nje ya line yetu ya umeme baadaye inaangukia ndani ya line yetu kwa sababu inakuwa ni mirefu sana. Kwa hiyo, tumeendelea kufyeka na kuhamasisha wananchi basi hata watuongezee line ambayo iko nje zaidi ya line yetu sisi ili tunapofyeka basi miti inayotokea nje ya line
yao isije ikaleta shida kwenye eneo letu.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ambalo linatupa shida sana kwa Mkoa wa Njombe ni radi. Maeneo ya Njombe, kama nilivyowahi kusema hapa, Mkoa wa Kagera lakini pia Mbeya, tunayo matatizo makubwa sana ya radi ambazo zimekuwa zikileta shida kwenye miundombinu yetu ya umeme.

Mheshimiwa Spika, tunachokifanya kwa Mkoa wa Njombe kwa mfano kila tunapofunga transformer tunaifanyia earthing system. Ile earthing system inatakiwa uzamishe chini, lakini unapima udongo kuona resistance value ya udongo ni kiasi gani. Kama iko 0 - 60 inakuwa haina shida, kama iko zaidi ya 60 inabidi kutumia zile njia za kienyeji na za kitaalam za ku--treat udongo ili radi ikienda iweze kumezwa kule, tunatumia mbolea na vitu vingine kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, pengine tukifunga transformer tunachelewa kuiwasha kwa sababu tukipima resistance value ya udongo tunaona bado ina-resist sana radi, kwa hiyo, tunaamua kuiacha kwanza ili ipoe kidogo.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba nimalizie. Naomba niruhusiwe kutoa nondo kama alizozitoa mwenzangu Ndaisaba jana kwa ajili ya uelewa mzuri.

Mheshimiwa Spika, lakini eneo la pili tunafunga vifaa vya muhimu sana vinavyoitwa surge arrester and combi unit kuhakikisha kwamba transformer haiharibiki mara kwa mara. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Deo kwamba tutaendelea kuhakikisha kwamba…

SPIKA: Nakushukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri.
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, nataka kujua ni sababu zipi zinazosababisha kusuasua kwa usambazaji wa gesi kwa matumizi ya binadamu katika Mkoa wa Mtwara hususan Manispaa ya Mtwara Mikindani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, sisi watu wa Mtwara kabla hatujapata gesi kwa matumizi yetu, gesi imepelekwa Dar es Salaam na watu wameunganishiwa majumbani. Kwa nini wameanza Dar es Salaam badala ya Mtwara ambako gesi inatoka kwa sababu na sisi pia tuna matumizi nayo? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza kwa pamoja ya Mheshimiwa Tunza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kusema kwamba usambazaji wa gesi katika Mkoa wa Mtwara hausuisui. Tulianza kuzalisha gesi katika Mkoa wetu wa Mtwara mwaka 2015 na mpaka sasa tunatumia umeme wa gesi peke yake kwa Mkoa wa Mtwara, Lindi na mikoa mingine yote ya Kusini. Umeme wote unaotumika kule unatokana na nishati ya gesi. Mpaka kufikia mwezi Julai mwaka huu, tayari nyumba 425 zitakuwa zimeunganishwa na huduma ya gesi majumbani kwa ajili ya matumizi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ambalo ni la kufurahisha, watumiaji wakubwa sana wa gesi Tanzania wa kwanza ni TANESCO na wa pili ni kiwanda chetu cha Dangote ambacho kiko Mtwara. Kiwanda hicho kinatoa ajira kwa vijana wetu, watu wanalipa kodi na Serikali inapata manufaa makubwa sana. Kwa hiyo, ni mojawapo ya faida kubwa sana ambayo inapatikana kule. Tunazo taasisi kama nne, Magereza, VETA, shule moja ya sekondari na chuo kingine kimoja, zinatumia gesi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, napenda kusema kwa kweli Serikali imejitahidi sana kuhakikisha wananchi wa Mtwara wananufaika na nishati hii. Hata hivyo, kwa sababu nishati ni kwa ajili ya Watanzania wote basi nyingine kidogo inatoka na kwenda kwingineko mpaka hapa Dodoma tutaweza kuifikisha kwa wakati. (Makofi)
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo mawili ya nyongeza. Kabla sijauliza maswali yangu, naomba tu niweke wazi kwamba sijaridhishwa na majibu ya Serikali kwa swali langu kwa sababu nilitegemea kwamba nitapewa mchanganuo wa hii bilioni 11.33 kwa kuonesha katika kila kijiji ni watu wangapi wamefidiwa kiasi gani na kiasi gani kimekwenda kwenye maendeleo ya vijiji husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini haiishii hapo Kijiji hiki cha Engikaret mahesabu yake hayapo katika jibu moja kwa moja. Ukiangalia hiyo bilioni 11.33 kwa mchanganuo uliotolewa inaonesha ni shilingi bilioni 1.669 tu ndiyo imefika na hiyo bilioni 9.660 sijaelewa kwamba mahesabu yake yamekwenda wapi.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo swali langu la kwanza la nyongeza ni kuhusu kijiji cha Engikaret. Kwa kuwa, kulikuwa na wananchi 46 ambao walileta malalamiko yao kwamba wako kwenye njia ya umeme na wakaenda wakafanyiwa tathmini na kuna wengine 66 waliletwa hivi karibuni.

Je, watu hawa ambao kwa ujumla wao sasa ni zaidi ya watu 112 watalipwa lini hiyo fidia?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kuna umeme ambao ulielekezwa Tarafa ya Ketundeine, umeme wa REA ukifanywa na kampuni yetu ya TANESCO. Kasi ya umeme huo ni ndogo sana na tulitegemea mwezi Julai mwaka jana ungewashwa katika vijiji 10 vya awali kwenye Tarafa hiyo yenye vijiji 19. Je, umeme huu wa Ketundeine utakamilishwa lini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Dkt. Steven, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji mkubwa ambao ameendelea kuufanya katika eneo lake. Niseme tu kwamba huo mchanganuo aliousema wa item moja moja kwa ajili ya wananchi baada ya hapa nitauagiza utengenezwe na nitaweza kumpatia kwa ajili ya kuona nani amelipwa nini ili aweze kuwasemea wananchi wake vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika eneo la malipo nieleze tu kwamba tulipata changamoto kidogo. Katika kijiji cha Engikaret tulivyofanya tathmini mara ya kwanza ilionekana kwamba ni eneo la kijiji lakini wakati pesa imekwenda kulipwa wakaja wananchi wengine takriban 40 na zaidi wakasema wana haki katika eneo hilo na sisi tukawafanyia tathmini kutoka kwenye ile ya kijiji ili wao walipwe. Kabla ya pesa ile haijalipwa wakajitokeza wananchi wengine zaidi ya 50 wakiwa na malalamiko hayo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na hali hiyo, yakawepo makubaliano kati ya TANESCO na Ofisi ya Mkurugenzi na Mkuu wa Wilaya kwamba kwa kuwa lile eneo lote lilifanyiwa tathmini likiaminika ni la Serikali basi Ofisi ya Mkuu wa Wilaya na Halmashauri zitathmini ni nani anastahili kulipwa nini katika eneo hilo na pesa ile ambayo tayari ipo katika akaunti ya Halmashauri iweze kutumika kwa ajili ya malipo hayo. Kwa hiyo, nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge, pesa tayari imeshalipwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri na yeye anaendelea na utaratibu wa kuhakiki ni nani anastahili kulipwa kama mmojawapo wa wale ambao wako katika eneo hilo.

Katika swali la nyongeza la pili, ni kweli kwamba mradi huo wa vijiji 19 umechelewa. Tulikubaliana na mkandarasi ukamilike kabla ya mwezi Juni mwaka huu na siku siyo nyingi Mheshimiwa Waziri wa Nishati atakuja kuzindua mradi huo kabla ya Mwaka huu wa Fedha kuisha.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Kwanza kabisa, nakupongeza kwa kurudi kwenye hicho kiti, tuliku-miss sana Mzee wa Jaza Ujazwe. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa majibu ya Serikali lakini nina maswali mawili ya nyongeza na msingi wa maswali haya ya nyongeza la kwanza, asilimia thelathini ya muda wa kufanya kazi katika Mji wa Mafinga na maeneo yanayozunguka unapotea kutokana na kukatikakatika kwa umeme. Hii maana yake ni nini? Saa za kufanyakazi katika nchi yetu wastani kwa mujibu wa sheria ni saa nane. Kwa hiyo, kwa siku tunapoteza wastani wa saa mbili au dakika 144, kwa wiki tunapoteza wastani wa saa 16 au dakika 1008, kwa mwezi tunapoteza saa ya kufanya kazi 40 au dakika 2,400. Maana yake ni kwamba tunapoteza kwanza mapato kwa TANESCO yenyewe lakini pia mapato kwa wananchi na kwa Serikali. Swali langu linakuja, kama tuna viwanda vikubwa 80 kwa nini tusiwe na Wilaya ya TANESCO katika Mji wa Mafinga kama ambavyo katika Wilaya ya Ilala, Wilaya ya Temeke, Wilaya ya Kinondoni wana Wilaya za TANESCO zaidi ya moja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, toka asubuhi nimepokea simu na meseji nyingi sana kutoka kwa wananchi wakiuliza kwamba wanashindwa kununua LUKU leo siku ya pili jambo ambalo linakosesha TANESCO mapato lakini pia shughuli za uzalishaji kwa wananchi kukosa umeme zinakuwa zimesimama. Nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Chumi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza Mafinga ni mojawapo ya maeneo ambayo TANESCO inafanikiwa kwa asilimia kubwa kupeleka umeme wa uhakika, kwa sababu inayo sub-station ambayo ipo jirani kilometa kama 80 kutoka kwenye huo mji wenyewe eneo la Igowolo na umeme huo unatokea Iringa.

Pia tunayo line nyingine ndogo inayotoka Iringa moja kwa moja kupeleka umeme Mafinga. Kwa hiyo, Mji wa Mafinga unalishwa na line mbili za umeme, ikitoka moja inaunganishwa nyingine, ikitoka nyingine inaunganishwa hiyo moja. Kwa hiyo, nimuombe tu Mheshimiwa Chumi aendelee kutuvumilia katika maboresho tunayoendelea kuyafanya kuhakikisha umeme unakuwa wa uhakika na kama ambavyo tumeshasema mara kwa mara eneo la Iringa, Mafinga, Mbeya na Bukoba tunaathari sana za kupatwa na radi kwa hiyo tunaendelea kurekebisha mifumo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili la LUKU, nikiri kwamba kwa siku mbili na leo itakuwa ni ya tatu tumekuwa tuna tatizo na tumepata shida kubwa sana kwenye mfumo wa kidigitali wa kununua na kuuza LUKU. Tunawahakikishia kwamba tunalishughulikia, tunazo system mbili; system moja imekufa, ilipata hitilafu kidogo na tayari tumeshapata itengenezwe na hiyo system nyingine iliyobakia inabeba mzigo mkubwa sana na hivyo inashindwa kuhudumia wateja wote kwa wakati. Tunaahidiwa na wataalamu wetu kwamba kabla ya siku ya leo haijaisha tatizo hilo litakuwa limekwisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge na kupitia forum hii, naomba niwaambie Watanzania wote kwamba ukifika katika ofisi za TANESCO unaweza ukanunua umeme. Shida tunayo kwenye ile data base au mfumo unaouza kupitia kwenye mifumo ya kibenki na mifumo ya simu, ile ndiyo imepata shida kidogo lakini ukifika Ofisi ya TANESCO unaweza ukanunua umeme. Naomba radhi kwa niaba ya wenzangu lakini tunawahakikishia kwamba leo kabla siku haijaisha tutajitahidi kuhakikisha huduma hiyo inarejea ili Watanzania waendelee kupata huduma ya LUKU kama kawaida.
MHE. LUCY T. MAYENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpango wa usambazaji wa umeme kwa kutumia REA umekuwa ukitumia transfoma za KV 50 lakini Serikali kwa ujumla na kama Taifa tumekuwa tukihamasisha sana shughuli za uzalishaji. Je, Serikali haioni kwamba kwa kuendelea kutumia umeme huu wa KV 50 wakati idadi ya watu na shughuli za uzalishaji zinaongezeka baadaye kuonekana kwamba umeme huu hautoshi. Kwa nini Serikali isianze sasa kubadilisha badala ya kuweka KV 50 ianze kwa maeneo kidogo kidogo kuweka KV 100? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lucy, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiwa tunapeleka umeme tunaangalia na kuzingatia mahitaji ya wananchi walio katika maeneo hayo. Transformer ya KV 50 ni transformer kubwa inaweza kuhudumia wateja zaidi ya 200 katika eneo moja. Kwa hiyo, kadri wateja wanavyoongezeka na sisi tutazidi kuboresha na kuongeza ukubwa wa transformer tunazoziweka katika maeneo husika.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Hii Kata ya Ugalla na huo mradi anaosema umeanza mwezi Machi, lakini hakuna dalili yoyote ya mradi, hakuna kitu chochote; na wananchi katika kata hiyo wamesubiri kwa muda mrefu, ni kata; kuna Kata ya Litapunga na Ugala wana miaka mingi wanaona wenzao wanapata umeme lakini wenyewe hawajawahi kupata umeme wala dalili ya nguzo hamna, lakini hapa ameniambia kuwa mwezi Machi mradi umeanza. Sasa hapo kidogo napata wasiwasi kwa sababu hamna dalili kabisa, hakuna dalili ya umeme. Sasa naomba basi Naibu Waziri aji-commit twende akaone ili ajue hali halisi ya wananchi kwa jinsi wanavyopata tabu.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; wananchi katika vijiji vingine wanalipia umeme Sh.27,000, lakini wanachukua muda mrefu sana miezi sita, saba mpaka nane hawaingiziwi umeme, basi Waziri atueleze wakilipa inachukua muda gani ili wananchi wanaweza kupata umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Lupembe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi wa upelekaji umeme wa awamu ya tatu, mzunguko wa pili, ulisainiwa na kuzinduliwa rasmi mwezi Machi na hatua kwa hatua zimekuwa zikianza sehemu moja moja kuendelea. Kwa mfano Mtwara wameendelea, Jumamosi iliyopita Mheshimiwa Waziri alizindua tena Arusha, kwa hiyo kufikia Disemba mwakani ndio maeneo yote yatakuwa yamekamilika. Kuna maeneo mengine yameshaanza, mengine bado yanaendelea, lakini hatua za kupeleka nguzo zimeanza. Kwa hiyo uzinduzi ndio ulikuwa mwezi Machi mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, kwenye maeneo mengine kama alivyosema kwake, watu wanapolipa umeme zinachukuliwa zile hatua sasa za kupeleka vifaa mbalimbali kwa wale wananchi waliolipia kama nguzo kama waya kwa pamoja ili sasa tuweze kufunga kwa pamoja. Hata hivyo, tunachofanya tunaweka utaratibu angalau tuseme ndani ya mwezi mmoja, kila mtu aliyelipia umeme awe ameupata kulingana na mazingira aliyokuwa nayo. Pengine kwenye three phase inachukua hadi pengine siku 90, lakini tumekuwa tukijitahidi kuhakikisha kwamba kila aliyelipia umeme anaupata na anaupata kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nimpongeze Mheshimiwa Mbunge na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa jibu lake la msingi.

Mheshimiwa Spika, ni kweli utelekezaji wa mradi kambambe wa awamu ya tatu, round ya pili umeanza rasmi toka mwezi Machi mwaka huu na wakandarasi wote wameshakwenda site. Kesho tuna mkutano wa wakandarasi wote hapa Dodoma, kuwaarifu watoe taarifa kwa Waheshimiwa Wabunge na Madiwani katika maeneo yao. Kwa hiyo inawezekana Mheshimiwa Mbunge kweli hajakutana nao, lakini wameshaanza kazi rasmi na wanakwenda kila eneo kwenye maeneo ambako wamepangiwa kazi.

Mheshimiwa Spika, nitoe taarifa tu kwa wakandarasi kupitia Bunge lako Tukufu kwamba, wakandarasi wote wakaripoti kwa Waheshimiwa Wabunge wanapoingia katika maeneo yao ili Waheshimiwa Wabunge wapate taarifa hizo. (Makofi)
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kabla sijauliza maswali mawili ya nyongeza naomba kwanza nikushukuru sana pamoja na Serikali kwa changamoto ambazo tulizipata Jimbo la Busokelo kwa mafuriko ambayo yalisababisha nyumba zaidi ya 30 pamoja na mtu mmoja kufariki, lakini wewe pamoja na timu yako mlikuja kutoa msaada. Ahsanteni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza, pamoja na majibu ya Serikali, huu Mradi wa Mto Rumakali upo katika halmashauri mbili kati ya Halmashauri ya Busokelo pamoja na Mkoa wa Njombe, lakini mradi huu katika utekelezaji wake inaonyesha kwamba licha ya kwamba megawati hizo zitazalishwa tunahitaji kujua wananchi wa Busokelo, je, ni kwa kiwango gani kupitia Corporate Social Responsibility ya mradi huu watanufaika wananchi wa Busokelo pamoja na Kata hii ya Lufilyo? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kwa kuwa mradi huu utaanza kuzalishwa hivi karibuni na tunafahamu kwamba Halmashauri ya Busokelo ni halmashauri changa, je, ni kwa kiwango gani Serikali imejipanga kuboresha miundombinu kufikia sehemu ya uzalishaji wa mradi huu kupitia Halmashauri ya Busokelo hususani madaraja ya Mto Lufilyo pamoja na madaraja ya Mto Malisi? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Atupele, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapotekeleza miradi mikubwa ya namna hii kipande cha Corporate Social Responsibility kwa maana ya manufaa ya mradi kwa umma ni kipande ambacho kinaongozwa na sheria tuliyokuwa nayo kwetu Tanzania na tunakiweka kwenye mkataba kwa ajili ya kukubaliana kwamba katika mapato na kazi utakayoifanya kiasi hiki basi kirudi kurudisha huduma katika jamii husika. Tunakwenda afya, tunakwenda kwenye maji, tunakwenda kwenye elimu na kwenye miundombinu kama hiyo ya barabara.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ni katika mradi wetu wa Mwalimu Nyerere, katika mradi wetu ule tunazo trilioni sita, lakini asilimia nne zimeenda kwenye CSR kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutakapokuwa tumeingia mkataba na mkandarasi wa kujenga mradi ule, lazima tuwe na kifungu cha Corporate Social Responsibility ambacho kitawanufaisha wananchi wa Busokelo, lakini pia na Makete ambapo ndiyo bwawa linapoanzia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili, umuhimu wa kufikia ile miundombinu itakayotengenezwa ndiyo itakayofanya miundombinu ya barabara iwepo, kwa sababu mradi kama mradi kwa maana ya ujenzi wa bwawa, lakini pia ujenzi wa ile power house, sehemu ambayo umeme utazalishwa, lazima tuwe tuna barabara nzuri zinazopitika kwa sababu tunayo mizigo mikubwa ambayo tunatakiwa kuisafirisha kuifikisha katika maeneo yale. Kwa hiyo tutajenga barabara hizo ikiwa ni faida kwa kuhudumia mradi, lakini pia na kuhudumia wananchi wa maeneo hayo kwa ajili ya kufikika katika maeneo yote.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, kwanza niipongeze Wizara ya Nishati kwa sababu mradi huu wa Bwawa la Rumakali, bwawa linajengwa Wilaya ya Makete, lakini power plant inajengwa Busokelo kwa ndugu yangu Mwakibete.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu dogo la nyongeza lilikuwa Waziri alipokuja Makete mwezi wa kwanza aliahidi kwamba mradi huu utaanza mwezi Machi kwa maana ya demarcation kuweka alama, lakini hadi sasa haujaanza. Je, ni lini Serikali itaanza kuweka alama (demarcation) kwenye mradi huu ili wananchi waendelee na shughuli za kijamii, waachane na hii changamoto waliyonayo sasa wanashindwa kuendelea na shughuli za kijamii kwa sababu, hawajui bwawa mipaka itaishia wapi? Naomba pia kujua kuhusu mambo ya fidia. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mwezi Januari Mheshimiwa Waziri alitembelea mradi ule kuona maandalizi yake yamefikia wapi na sisi kama Serikali tumejipanga kuanzia tarehe Mosi, mwezi Juni, wataalam wa Wizara na TANESCO wataenda katika eneo la mradi kwa ajili ya kuhakiki mipaka na kuweka demarcation na kufanya maandalizi ya kulipa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, fidia italipwa katika maeneo makubwa matatu. Fidia kwenye eneo ambapo litajengwa bwawa, lakini fidia katika eneo ambalo litaenda kuweka hiyo power house, sehemu ya kuzalisha umeme kwa sababu kutoka kwenye bwawa kushuka mpaka sehemu ya kuzalisha umeme kuna kilometa kama saba. Vile vile fidia italipwa kutoka kwenye njia ya kuzalisha umeme mpaka kwenye kituo chetu cha Iganjo ambapo kuna kilometa kama mia moja hamsini kutoka kwenye lile eneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo maeneo yote hayo kuanzia tarehe Mosi mwezi Juni yataanza kufanyiwa kazi ikiwa ni pamoja na kufanya tathmini kwa ajili ya kuweza kulipa fidia na mradi uweze kuendelea kama ilivyosemwa kufikia mwezi Oktoba.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, aya ya tatu ya jibu lako, kuna sehemu inasomeka hadi kituo cha kupooza umeme cha Iganjo Mkoani Mbeya. Sasa hiki kituo cha kupooza umeme hii Kata hii inayoitwa Iganjo mlipoweka kituo hiki cha kupooza umeme, Mtaa wa Igodima hauna umeme, sasa mmeweka kituo cha kupooza umeme, lakini mtaa hauna umeme. Huo mtaa utapata lini umeme? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru na kama tulivyokuwa tukieleza hapo awali ni nia ya Serikali kuhakikisha kila mwananchi wa nchi hii anapata umeme katika eneo lake. Katika eneo hili sasa ni eneo la kipaumbele kwa sababu siyo vema kumpelekea mtu shughuli ambayo wananufaika nayo wengine. Kwa hiyo, nitoe ahadi ya Serikali kwamba, tutahakikisha hicho kituo kinapowekwa pale basi tunaweza kupata umeme wa kuhudumia yale maeneo yote ya jirani kama ambavyo tumefanya hivi karibuni katika Bwawa la Mtera kwa kuongeza pale transformer ya kuhudumiwa wale wananchi wanaoishi katika maeneo yale kwa haraka kabisa.
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kunipa majibu ambayo pia nahitaji nipate uhakika.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa umeme ni chachu ya maendeleo na kwa kuwa ni asilimia 44 tu ya vijiji vya Singida Mashariki vina umeme, ninalotaka kujua na wananchi wa Singida Mashariki, hususan Tarafa ya Mungaa ambayo ina kata saba na ambayo haina umeme kabisa.

Ni lini mkandarasi atakwenda kuanza kazi kama alivyosema mwezi Machi mpaka sasa hajapatikana na tunataka tujue jina la mkandarasi huyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwa kuwa, vijiji ambavyo amevitaja anasema vina umeme na kwa sababu kuna mradi wa ujazilishaji na mpaka tunavyoongea sasa ni unaenda taratibu mno. Hawaoni sababu ya kuongeza kasi ya kuweza kuweka umeme katika vitongoji vilivyobaki? (Makofi)

SPIKA: Yaani Mheshimiwa Mtaturu kuna tarafa ambayo haina umeme, tarafa nzima?

MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, Tarafa nzima ya Mungai yenye Kata za Mungaa, Lighwa, Makiungu, Kata ya Ituntu, Mungaa na Kikiyo pamoja na Kata ya Msughaa zote hazina umeme ambazo ni mpakani mwa Chemba.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mtaturu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunakiri ni kweli kwamba mpaka sasa kuna baadhi ya vijiji Tanzania havijafikiwa na umeme. Kama tulivyosema tulianza tukiwa na vijiji 12,268 lakini tumepunguza mpaka sasa tuna vijiji 1,974 ndio havina umeme na mpango uliopo kwa sasa ni kuhakikisha kabla ya mwezi Disemba, 2022 vijiji vyote hivyo 1,974 vyote vinakuwa vimepata umeme na tuko tayari tumeshawapata wakandarasi wa kupeleka umeme kwa kila eneo katika REA III, Round II.

Mheshimiwa Spika, Jumanne ya wiki hii tulikuwa tuna kikao na wakandarasi hao ambao tuymewapa kazi hizo na tumewaagiza kabla ya Jumatatu inayokuja wawe wote wamewapigia simu Waheshimiwa Wabunge pamoja na viongozi wengine kwenye maeneo kuwaambia kwamba tumekuja na tumeripoti kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Waziri juzi kuna maeneo wakandarasi wetu wameenda, lakini hawakuwa wametoa taarifa ya kutosha kwa Waheshimiwa Wabunge ambao ni wawakilishi wa wananchi, ili kuweza kujua kwamba wapo. Sasa mimi nimechukua jitihada ya kuwapatia wakandarasi namba za Waheshimiwa Wabunge na kuwaelekeza kabla ya Jumatatu nitakuwa nime-verify kwa Mbunge mmoja-mmoja kujua kama amepigiwa simu au kutumiwa message kuambiwa kwamba mimi ninaenda kuripoti katika eneo hilo. Kwa hiyo, niseme katika maeneo hayo ambayo Mheshimiwa Mtaturu ameyataja kazi inaendelea na tutafikisha umeme katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali la pili, kwenye densification (ujazilizi); mkandarasi anayeendelea kufanya kazi katika Mkoa wetu wa Singida anaitwa Sengerema, ni mkandarasi mzuri, anafanya kazi yake vizuri na anakwenda hatua kwa hatua na tunatarajia kufikia mwezi Disemba mwaka huu atakuwa amemaliza vitongoji vyote. Kwenye kupeleka umeme kwenye vitongoji tunapaleka kupitia miradi yetu ya REA ambao wanapeleka kwenye vijiji wanashuka kwenye vitongoji, lakini tuna mradi maalum huu wa densification ambao wenyewe unalenga vitongoji, lakini pia na wenzetu wa TANESCO bado wanalenga vitongoji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kufikia mwaka 2022 tunatarajia kuwa tume-cover vijiji vyote, lakini tunakuwa tume-cover vitongoji vingi sana. Mpango wetu kuendelea kupeleka umeme katika vitongoji kwa sababu kupeleka umeme ni zoezi endelevu.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nipongeze majibu ya nyongeza ya Mheshimiwa Naibu Waziri katika Jimbo la Mheshimiwa Mtaturu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli jimbo la Mheshimiwa Mtaturu kimsingi ile tarafa ambayo haijapata umeme pamoja na tarafa nyingine zote wakandarasi wameondoka jana kwenda Singida kwenda kufanya kazi, pamoja na tarafa hiyo. Mheshimiwa Mtaturu alikuwa na vijiji 12 ambavyo havijaguswa kabisa pamoja na hiyo tarafa.

Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mtaturu pamoja na Waheshimiwa Madiwani na Waheshimiwa wananchi wa Singida katika jimbo lake wote watapata umeme ndani ya miezi 18 kuanzia jana walipoondoka wakandarasi. (Makofi)
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru pamoja na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri tuishukuru Serikali kwa kazi ambayo imeanza kwenye vile vijiji vichache viwili ambavyo vilikuwa vimepitiwa na umeme mkubwa, lakini kwa hivi vijiji 47 kwa kuwa tunategemea Mradi wa REA, kazi hii Mheshimiwa Naibu Waziri imekuwa na changamoto kidogo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kupata majibu ya Serikali sasa ni lini kazi za kupelekea umeme kwenye vijiji hivi vyote vilivyobaki itaanza na kukamilika kwa ajili ya manufaa ya wananchi wa Jimbo la Korogwe?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili kwenye Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko ule wa Kwanza tulipeleka umeme kwenye vijiji, lakini maeneo mengi ya vijiji bado hajafikiwa na kwenye mzunguko huo wa pili tunafikiria kupeleka kwenye kilometa moja kwenye kila kijiji.

Ni upi mpango sasa wa Serikali kwa vile vijiji vya mzunguko ule wa kwanza na ule mzunguko wa pili kukamilisha maeneo yote ya vijiji ili wananchi wa vijiji vyetu waweze kupata huduma hii ya umeme? Nashukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema katika majibu ya msingi kwamba upelekaji wa umeme kwenye vijiji vyote 49 na hivyo viwili tayari kazi imeanza, itakamilika ifikapo Septemba, 2022 na niseme ni kwa Korogwe Vijijini peke yake lakini katika maeneo yote ambayo vile vijiji tulikuwa hatujavipelekea umeme tayari kazi hizi zimeanza na tutahakikisha kwamba ndani ya huo muda tuliousema ambao maximum ni Disemba, 2022 vijiji vyote kama 1,500 vilivyobakia vitakuwa vimepata umeme na tutahakikisha kwamba kila mtu anapata manufaa ya umeme huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika swali la pili ni kweli kwamba mpaka sasa hatujatosheleza kupeleka umeme katika vitongoji vyote kwenye maeneo yote, lakini maendeleo ni hatua, tulianza hatuna kabisa, sasa tumepeleka robo, baadaye nusu, sasa kwenye vijiji tunaenda kumaliza. Niwaahidi tu Waheshimiwa Wabunge kwamba Serikali inayo nia ya dhati ya kuhakikisha kwamba katika vitongoji pia tunafikisha umeme kwa kadri inavyowezekana, na kama tulivyokuwa tunasema kwenye vitongoji tunapeleka kupitia hiyo REA, lakini huko mradi maalum wa kupeleka umeme kwenye vitongoji unaoitwa densification, lakini pia TANESCO ni jukumu lao la kila siku kuhakikisha wanapeleka umeme katika maeneo hayo, ni wahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba tutaendelea kupeleka umeme katika maeneo yote ya nchi yetu ya Tanzania.
MHE. DKT. ASHATU K. KIJAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunahitimisha mahojiano na Waziri akatuambia kwenye utekelezaji wa REA Awamu ya Tatu vijiji vyote vinakwenda kupata umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachoendelea kwenye vijiji vyetu na majimbo yetu ni mchakato ambao haueleweki kwa wananchi kwa sababu walimsikia Waziri akisema kila nyumba, kila kijiji na kila kitongoji kinakwenda kupata umeme. Kinachoendelea kwa wakandarasi walioki site sasa wanafanya survey wanasema kila kijiji wanapelekea nyumba 20 tu, sasa hii imeleta changamoto kwetu sisi Wabunge hasa tunaotoka vijijini.

Ni nini kauli ya Serikali wao ili wawaeleze wananchi ni nyumba zote vijiji vyote au tunakwenda awamu kwa awamu? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ashatu Mbunge wa Kondoa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba kila Mtanzania anapata umeme nyumbani kwake, lakini haiwezi kuwezekana kufanya hivyo kwa siku moja na tunapotoa kazi kwa mkandarasi kulingana na bajeti na fedha tuliyonayo tumekuwa tukianza na wale tunaowaita wateja wa awali kwa hiyo mkandarasi tunampa kazi ya kupeleka umeme katika eneo fulani, na kwenye mkataba wake tunampa labda wananchi 100 au 500 au 700 kulingana na wigo wa lile eneo lilivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mkandarasi akikamilisha hao watu 500 sisi tunafunga mkataba wa mkandarasi kwamba tunamaliza.

Sasa kinachokuwa kimebakia ni kwamba wananchi wa maeneo yale sasa waendelee kufuatilia na kuomba umeme kutoka taasisi yetu ya umeme yetu ya TANESCO ili waendelee kuunganishiwa kwa sababu sio watu wote wanakuwa tayari kuunganishiwa umeme katika siku moja ambapo mkandarasi anakuwepo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kwa maelezo mafupi ni kwamba mkandarasi anakuwa na wateja wa awali wa kuanza nao na akikamilisha wale aliopewa wateja wengine wanaendelea kupewa umeme na TANESCO na tutahakikisha kwamba kila Mtanzania anapata umeme nyumbani kwake. (Makofi)
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni lini Serikali itakamilisha kupeleka umeme katika vijiji vya Halmashauri ya Wilaya ya Mpanda, vijiji ambavyo viko katika Kata ya Kakese, Kijiji cha Kamakuka, lakini katika Kata ya Mwamkulu vijiji kama Saint Maria, Kawanzige, Mkwajuni na Ikokwa, lakini katika Kata ya Kakese, Kijiji cha Songebila? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Martha Mariki, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Katavi kwamba vile vijiji vyote alivyovitaja kikiwemo cha Saint Maria ambayo nimekisia vizuri vyote viko katika mpango wa REA III Round II na tayari mkandarasi ameshaaza kazi katika maeneo hayo tunamshukuru kwa sababu yeye na Mheshimiwa Pinda wamekuwa wakifuatilia na tunahakikisha kwamba kabla ya Disemba mwakani tayari vijiji hivyo vitakuwa vimepata umeme kwa ile programu tuliyoiweka ya mkandarasi kuhakikisha anapeleka umeme katika muda huo.
MHE. KABULA E. SHITOBELO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Je, ni lini Serikali itakamilisha kazi ya kupeleka umeme katika vijiji vya Mkoa wa Mwanza kama Nyanchenche -Segerema; Nyakafungwa - Buchosa; Gulumungu - Misungwi; Kawekamo, Mwambogwa, Kwimba na Ilemela?
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kama ambavyo nimeeleza katika majibu ya muda uliopita na Mheshimiwa Naibu Waziri ulivyosema Mkoa wa Mwanza umebakiza vijiji 121; lakini yako maeneo ambayo ameyataja Mheshimiwa Mbunge maeneo la Ilemela, Nyamagana, Nyamadoke, Nyamongolo pamoja na maeneo yote ya Rwanima tutawapekelea umeme mwezi disemba mwaka unaokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini nimpe tu taarifa Mheshimiwa Mbunge kwamba Mwanza tumepeleka wakandarasi wa aina mbili; wakandarasi wa peri-urbun wanaendelea na maeneo uliyotaja, lakini kuna maeneo ya vitongoji ambayo yana-cover Sengerema mpaka Buchosa ambao wakandarasi wameshafika site tayari. (Makofi)
MHE. SILYVESTRY F. KOKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali kwa sababu kwa kweli kwa kipindi kifupi imefanya kazi nzuri na hasa ilivyoondoa mkanganyo wa ulipaji wa kufungiwa umeme kwa wananchi ili tunalishukuru sana Serikali yetu imefanya vizuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Kibaha bado tuna matatizo makubwa ya kusambaziwa umeme kwa wananchi na hususani katika mitaa ya Viziwaziwa kwa maana ya Sagale Magengeni, Sagale kambini lakini Muheza pamoja na maeneo mengine ya Misugusugu kwa maana ya Zogohale na Miomboni pia vilevile Madina hadi Kiembeni toka 2016 baadhi ya wananchi bado hawajapata umeme.

Je, ni lini sasa wananchi hawa watawekewa umeme ili waondokane na adha ya kukosa umeme katika Mji wa Kibaha?

Swali la pili, toka mwaka 2014 wananchi wengi wa Jimbo la Kibaha mjini walisimamishiwa maendeleo katika maeneo yao ambayo kunategemewa kupita mradi wa umeme wa msongo wa Kilowatt 400 kutoka Kinyerezi kuelekea Chalinze wasifanye lolote ingawa hadi leo bado wengine wanaendelea hata kutozwa kodi za ardhi.

Je, ni lini wananchi hawa watapata fidia zao ili waweze kufanya maendeleo maeneo mengine na kuondokana na adha hii?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Koka Mbunge wa Kibaha kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba baadhi ya maeneo ya Mji wetu wa Kibaha hayajapata umeme lakini tayari Serikali imejitahidi kupeleka umeme katika hayo maeneo machache ambayo ni jitihada ya Mheshimiwa Mbunge katika kufanya ufuatiliaji wa kina kuhakikisha maeneo yote yanapata umeme. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba maeneo yote ya Kibaha yataendelea kupelekewa umeme kupitia mradi wetu wa Peri- Urban na tayari Mkandarasi huyo ameshaongezewa scope ya kazi kwa hiyo maeneo yote ya Ziwaziwa na mengine ambayo yametajwa na Mheshimiwa Mbunge yote yatafikiwa na umeme kadri tunavyozidi kuendelea mbele kwasababau ni jukumu la TANESCO na REA na Serikali kuendelea kupeleka umeme kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, ni kweli kwamba kuna maeneo ambayo yalitwaliwa na Serikali kwa nia ya kupitisha mradi wa Msongo wa kilovolti 400 kusafirisha umeme na sasa utakuwa unasafirishwa kutoka Chalinze kuelekea Kinyelezi kwa sababu uzalishaji mkubwa unafanyika katika maeneo ya Mwalimu Nyerere.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali tayari imetoa fedha kwa TANESCO takribani Billioni 29.6 na kuanzia Julai, Mosi fidia zitaanza kulipwa kwa wananchi wa maeneo ya Chalinze, maeneo ya Kibaha na maeneo ya Kinyerezi kwa ajili ya kupisha mradi huo uanze kujengwa mara moja.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, nashukuru pia kwa majibu mazuri ya Serikali yanayotia moyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sura ilivyo katika eneo la mradi kuna hali ya kusuasua, nilichokuwa naomba nafahamu uhakiki wa uwezo wa mtengenezaji kwa maana ya due- diligence jambo hili bado halijafanyika sambamba na utiaji saini mikabata, nilikuwa naiomba Serikali inihakikishie ni lini suala hili litafanyika ili kuharakisha mradi huu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kapufi wa Mpanda kama ifuatavyo, kama tulivyosema katika swali la msingi ni kwamba tayari ujenzi umeanza kwenye maeneo hayo na vituo vya kupoozea umeme tayari vimetengenezwa na majengo yake yamekamilika kwa asilimia 90, ni kweli kwamba uhakiki wa uwezo wa Mkandarasi wa kututengenezea vile vifaa vya ndani ya kile chumba cha kupoozea umeme vikiwemo generator, transforma na vitu kama hivyo broker na breakers nyingine haujafanyika vizuri kwasababu ya tatizo kubwa ambalo liliwapata wenzetu ambao wanaweze kututengenezea vifaa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ni vigumu kwetu sisi kutuma wataalam wetu kwenda kwenye hizo nchi ambazo zinao watengenezaji wa vifaa hivi vikubwa kwenda kuhakiki uwezo wa watengenezaji hao. Lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ufuatiliaji wake sisi kwetu ni faraja na tunaelekea kukamilisha kwa sababu tayari sasa nchi ambazo zinatengeneza vifaa hivi zimeanza kuruhusu watu mbalimbali kwenda kufanya shughuli mbalimbali kwenye nchi zao baada ya janga la Korona kupungua kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajiandaa kutuma wataalam wetu kwenda kuhakiki kama wale tuliowapa kazi wana uwezo wa kutengeneza hizo mashine tunazoziomba na baada ya hapo mikataba itasainiwa kama tulivyosema kwenye jibu la Msingi kwamba 2023 mradi huu utakuwa umekamilika na grid ya Taifa itafika Mpanda.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, toka mradi wa REA-I na REA- II katika Wilaya ya Kyela Vijiji vya Lupaso Ndondwa na Mabuga mpaka sasa hawajapata umeme.

Je, nini jitihada za Serikali kuhakikisha tunapata umeme maeneo hayo. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli yapo baadhi ya maeneo ambayo REA I na REA II ilikuwa haijakamillisha, kulikuwa na changamoto mbalimbali ambazo sasa tumezitafutia mkakati maalum wa kuzimaliza na tunahakikisha kwamba inapoelekea 2022 tunapomaliza REA III round II na vile viporo vyote vya nyuma tutakuwa tumevimaliza, yalikuwepo matatizo ya Wakandarasi kushindwa kumalizia kazi kwa sababu ya changamoto mbalimbali lakini sasa tatizo hilo tumelitibu na tutahakikisha kwamba kila mwananchi anapata umeme katika maeneo yote ambayo yamepitiwa na mradi kulingana na scope ilivyokuwa kufikia 2022 kama ambavyo tumesema.
MHE. DAVID M. KIHENZILE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili la hali ya Mufindi linafanana pia na hapa mtangulizi amezungumza lakini tofauti ni kwamba asilimia 70 ya nguzo katika nchi hii zinatoka pale kwenye Jimbo letu, sasa ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye maeneo ambayo ni ya giza pamoja na kwamba nguzo zinatoka pale, especial maeneo la Idete, Maduma pamoja na Idunda na vijiji vya Kisasa na maeneo mengine ambayo hayana umeme kabisa na wanashuhudia nguzo zikipita kila siku mbele yao. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimwa Kihenzile Mbunge wa Mufindi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba tunakiri kuna maeneo bado hayana umeme mpaka sasa, Mufindi ni eneo mojawapo ambalo mkandarasi wa REA III round II tayari amepatikana MS Servicies na tayari ameenda kufanya survey kwenye maeneo husika, tunamhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba utuatiliaji wake ambao amekuwa akiufanya mara kwa mara utazaa matunda na tutapeleka umeme katika vijiji vyote alivyovisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo lazima lipewe kipaumbele na heshima kwa sababu ndiyo linalisha na maeneo mengine yanayotumia nguzo za miti, kwa hiyo kweli katika hali ya kawaida siyo kitu cha kufurahisha kuona unatoa bidhaa halafu wewe haunufaiki nayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla ya mwaka 2022 kukamilika tutakuwa tayari tumefikisha umeme katika maeneo yote ambayo hayana umeme. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nishukuru Serikali kwa kupeleka mkandarasi amesharipoti tarehe 11 Mwezi huu. Kwa kuwa Serikali inaenda kutekeleza mradi huu katika vijiji vyote vya Jimbo la Tunduru Kusini na Tunduru kwa ujumla na tatizo la Umeme Tunduru kukatika katika ni jambo la kawaida.

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga substation pale Tunduru Mjini ili kutoa huduma hii kwa vijiji vyote kwa sawasawa? (Makofi)

Swali la pili, kwa kuwa REA imeanza kutekelezwa katika vijiji vyote vilivyopo Jimbo la Tunduru Kusini pamoja na vijiji vya Azimio, Semeni, Angalia Je, Serikali sasa haioni kuna haja sasa ya kuweza kutoa tamko la kuweza kuisaidia TANESCO kwa asilimia 100 ili waweze kutoka huduma hiyo kwa shilingi 27,000?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Daimu Mpakate Mbunge wa Tunduru kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza kuhusu hoja ya kupeleka substation tuichukue tukaifanyie mkakati na upembuzi yakinifu na kuona kama ujenzi wa substation peke yake ndio utasaidia kutokatika kwa umeme katika maeneo hayo au njia nyingine inaweza ikaboresha kwa sababu pengine kama umeme unaofika ni mkubwa wa kutosha maana yake tunatakiwa kuboresha miundombinu badala ya kujenga substation. Tunalichukua tutaenda kulifanyia kazi na tutaweza kufikisha huduma nzuri kabisa kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika swali la pili tayari Serikali imeshatoa maagizo na maelekezo ya kuunganisha umeme kwa wateja wote kwa shilingi 27,000, katika bajeti iliyowasilishwa na Wizara ya Nishati kwa niaba ya Serikali ilisemwa hapa wazi na Mheshimiwa Waziri kwamba maeneo yote itakuwa ni shilingi 27,000 isipokuwa Dar es Salaam City Centre. Tayari wenzetu wa TANESCO wametoa circular kwa Meneja wa Wilaya na wa Mikoa kuhakikisha kwamba agizo hilo linatekelezwa na tunafahamu linaendelea kutekelezwa, lakini pale Waheshimiwa Wabunge ambapo bado mnaona changamoto basi tuwasiliane ili tuweze kuchukua hatua kwa sababu mambo mengine yanahitaji kusimamiwa kwa ajili ya manufaa ya wananchi. (Makofi)
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii niweze kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Simiyu una vijiji 470 na vijiji vilivyopata umeme ni 332 vimeshapata umeme vijiji vilivyobaki ni 138.

Je, ni lini Serikali itakamilisha kupeleka umeme katika vijiji vilivyobaki. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Midimu, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Simiyu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema ni kweli kwamba kuna maeneo bado hayajapata umeme katika vijiji takribani kama 1,500 nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba hivyo vijiji 132 ambavyo bado havijapata umeme kwa Mkoa wa Simiyu na vyenyewe vitapelekewa umeme kabla ya mwezi Desemba 2022 kwa sababu tayari mkandarasi tumempata na tunaamini amesharipoti site yupo katika hatua za kwanza za kufanya survey kuhakiki kwamba vijiji vimechukuliwa na baada ya hapo kazi itafanyika kwa muda uliopangwa na kukamilisha umeme kufikia Desemba 2022. (Makofi)
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa swali la nyongeza; lakini vile vile, naomba niishukuru sana Serikali kwa kweli kwa kazi kubwa iliyofanya ya kusambaza umeme vijijini. Ninashukuru sana ya kwamba vijiji 39 vya mwisho sasa navyo kazi imeshaanza ili kukamilisha vijiji vyote vya Wilaya yetu ya Mbeya, Halmashauri ya Mbeya Jimbo la Mbeya Vijijini kupata umeme, nashukuru sana kwa hilo; ingawaje mkandarasi alipewa vijiji 32 kwa hiyo nitamuomba Mheshimiwa Waziri ajaribu kuangalia ili kuoanisha hayo mahesabu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kazi nzuri sasa naomba niulize maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali kwa mradi mkubwa wa Tanzania Zambia Inter-Conector ambao unapita kwenye vijiji vya kata nane za Wilaya ya Mbeya Jimbo la Mbeya Vijijini. Inapita katika Kata za Ulenje, Inyala Maendeleo, Itewe, Swaya, Igale, Iwindi na Bonde la Songwe. Wananchi waliopisha ujenzi wa line hii waliahidiwa kupatiwa fidia tangu mwaka 2018, lakini mpaka leo hii wanasubiria hakuna kinachoendelea, na imekuwa kero kwa vile waliambiwa wasifanye ujenzi wala maendeleo yoyote. Sasa ni lini wananchi hawa watapata fidia yao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, kama unavyojua kupeleka umeme vijijini ni kuchochea uchumi, lakini kumekuwa na mkanganyiko wa tozo kati ya wateja wa line ya three phase na wateja wa line ya single phase. Wateja wa line ya three phase wanatozwa na TANESCO Shilingi 918,000 ambapo REA wanawatoza 139,000.

Je, Serikali ina mpango wa kuoanisha hizo tozo mbili ili kuchochea huo uchumi vijijini na wananchi waweze kulipia laki moja na thelathini na tisa badala ya laki tisa na kumi na mbili? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Manase Oran Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake na shukrani alizozitoa kwa Serikali, na mimi kwa niaba yake nizipokee, kwamba Serikali imejitahidi sana kuhakikisha inapeleka umeme vijijini na katika maeneo yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba vijiji 39 ambavyo anavyo vyote vitapata umeme pamoja na kwamba inawezekana mkandarasi alipewa 32 vya kwanza. Pia niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kwamba hata kama mkandarasi alipewa vijiji pungufu ya vile ambavyo uhalisia vimebaki, katika survey hii ambayo tumewatuma wakandarasi wafanye kwenye maeneo yetu watahakikisha na vile vijiji vingine ambavyo vilibaki au viliachwa vinachukuliwa katika kazi zao na katika adendum za nyongeza za kazi tutakazo wapatia, watavichukua vijiji vyote na kuvifanyia kazi. kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba ufuatiliaji wake umefanikiwa na wengine pia umeme utapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la fidia itakayolipwa kwenye mradi mkubwa wa kuunganisha umeme wa grid kutoka Iringa kwenda Mbeya, Tunduma mpaka Sumbawanga, takribani kilomita kama 622, kazi hiyo ya umbembuzi yakinifu imefanyika imekamilika na sasa makabrasha ya ulipaji wa fidia ndiyo yanawasilishwa sasa kwenye ofisi zetu kwa ajili ya uhakiki na kuweza kulipa fidia hiyo. Kwa hiyo bajeti ambayo Mheshimiwa Waziri aliwasilisha hapa juzi imetenga kiasi cha kuanzia, zaidi shilingi bilioni moja kwa ajili ya malipo ya fidia ya eneo hilo, na tutaanza kulipa fedha hiyo kuanzia kwenye mwezi wa kumi na kuendelea kwa ajili ya kupisha sasa ujenzi wa mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, niombe kutoa maelezo na maelekezo kwa watumishi wenzetu. Serikali imesikia kilio cha Watanzania na tayari ilielekeza kwamba umeme katika maeneo yote utaunganishwa kwa shilingi 27 kwa umeme mdogo. Kwenye maeneo yetu ya vijiji Serikali imetoa msamaha wa kuunganisha line ya nguvu kubwa three phase kwa gharama ya shilingi 139,000 tu. Kwa hiyo, ninawaelekeza watumishi wenzetu wa TANESCO kwamba maeneo yote ya vijijini ambapo either ni TANESCO kapeleka umeme au REA imepeleka umeme, gharama ya kuunganisha umeme wa three phase ni shilingi 139,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo shilingi 912,000/= ni kwenye maeneo mengine ya mijini ambapo mradi wa REA wowote ule haujafika. Kwa hiyo ieleweke wazi kabisa, waheshimiwa Wabunge tunaomba tusaidiane katika usimamizi wa hili. TANESCO akiwa analeta umeme au REA analeta umeme mkubwa gharama yake ni shilingi 132,000 kwenye maeneo yetu ya vijijini. Ahsante.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Nina maswali madogo mawili. Swali la kwanza; pamoja na majibu mazuri ya Serikali yenye kutia matumaini, kwa wananchi wanaopitiwa na mradi huo, wananchi wa eneo la Kivavi na eneo la Majengo na kwa sababu, wamesubiri kwa muda mrefu sana zaidi ya miaka saba na huu sasa tunakwenda mwaka wa nane. Je, Serikali itakuwa tayari kusimamia kama ambavyo wamesema hapa, ndani ya mwaka 2021/2022 na kuhakikisha kwamba, wananchi hawa watalipwa kama ambavyo amesema kwenye jibu la msingi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali itasimamia namna ya kuwalipa fidia wakati wa kuwalipa utakapofika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika juhudi za Serikali za kuhakikisha inaongeza wigo wa umeme, tunazalisha umeme kutoka katika vyanzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na maji, mafuta na gesi ambayo imezoeleka. Hata hivyo, tunafanya vitu vinavyoitwa energy mix, ambavyo ni vile vyanzo jadidifu tunaviita renewables ambayo kuna upepo, jua na ile wanayoita joto ardhi. Sasa, kwenye eneo la Makambako imeonekana tunaweza tukapata pale, umeme kwa kutumia upepo katika hicho Kijiji cha Majengo tulichokisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatarajia kupata kama megawati 1,179 kutoka kwenye hizo renewables. Sasa, tumewakaribisha wawekezaji binafsi ili waweze kuwekeza katika eneo hilo ili isaidiane na Serikali katika kupatikana kwa umeme huo. Huo mkataba nilioutaja unaelekeza kwamba, yule mwekezaji binafsi anayekuja kuwekeza katika eneo hilo, yeye ndiye ata-acquire ardhi na kuweza kulipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa, nipende kutoa commitment ya Serikali, Mheshimiwa Deo amefuatilia sana kwa muda mrefu madai haya na malipo haya, nimhakikishie kwamba, tumefikia mwisho wa makubaliano na kutafuta wawekezaji katika eneo hili na Serikali itasimamia kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, kuhakikisha kwamba, mkataba unaingiwa katika kipindi hicho kilichotajwa. Pili, kuhakikisha kwamba, kila yule anayetakiwa kulipwa fidia analipwa fidia stahiki katika eneo lake, kulingana na hali halisi na sheria inavyoelekeza katika maeneo hayo. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Deo kwamba, wananchi wa Makambako wamefanikiwa na naendelea kuwasimamia vyema na kile wanachokistahili kukipata, watakipata kwa wakati. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, Mheshimiwa Stephen Byabato, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Kwanza tunaishukuru Serikali kwa mradi. Swali la kwanza; Kata za Kasansa, Mamba, Maji Moto, Mbede Mwamapuli, Chamalendi, Usevya na Kibaoni zinatumia umeme wa kutoka nchi ya jirani ya Zambia, umeme ambao hautoshi ni kilowatt 100. Tuliomba kupata umeme wenye kilowatt 500. Je ni lini Serikali itatuletea transformer zenye kilowatt 500?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwenye Mji ya Nyonga ambao ni Makao Makuu ya Wilaya ya Mlele umeme hautoshi kwa sababu umeme uliopo wakati unawekwa ulikuwa umewekwa kwa mahitaji madogo, mji umeongezeka, wananchi wanafanya biashara, wamefungua miradi ya ujasiriamali, ambayo ni mashine za kusaga na vitu vingine. Je, Serikali haioni umuhimu wa kutuongezea umeme wenye megawatt zaidi ya nne?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Taska Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru kwa kutambua juhudi za Serikali za kuhakikisha kwamba gridi ya Taifa inafika katika Mkoa wetu wa Katavi. Mkoa wa Katavi haujafikiwa na gridi lakini unapata umeme kutoka katika vyanzo viwili, Wilaya ya Tanganyika na Wilaya ya Mpanda Mjini wanatumia generator mbili ambazo ziko pale Mpanda mjini na mpaka sasa zinazalisha megawatt kama 5.87 hivi na umeme ule unatosha maeneo yale kwa sababu matumizi ya Mkoa wa Katavi kwa sasa kwenye yale maeneo ya mjini ni megawatt kama 5.2.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini chanzo cha pili cha umeme kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge ni umeme ule unaotoka Zambia unapita Sumbawanga unapita Namanyere unakuja kuingia sehemu ya karibu na Mpanda Mjini unakuja kuingia kwenye Wilaya ya Mlele kwenye hayo maeneo ya Mwamapuli, Maeneo ya Majimoto, Maeneo ya Kibaoni aliyoyataja ambayo sasa ndio umeme unaingia pale kutokea Sumbawanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inachokifanya kwa sasa cha kwanza kabisa inahakikisha kufikia 2023 imefikisha gridi ya Taifa katika Mkoa wetu wa Mpanda kutokea Tabora. Jambo la pili ambalo inalifanya ni kuhakikisha kwamba inaongeza uwezo wa hizo transformer.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wiki iliyopita transformer yenye uwezo wa kilowatt 400 imeongezwa katika Wilaya ya Mlele ili kuongeza nguvu kwenye hayo maeneo ya Kata za Mlele ambazo amezitaja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Mbunge afanye mawasiliano, atataarifiwa kwamba sasa hali ya umeme imetulia na sasa Katavi inaweza kuendelea vizuri wakati tukiwa tunahakikisha kwamba gridi inafika kwenye Mkoa wetu wa Katavi.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi; pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Kwa kuwa Kata za Rungwa, Ipande na Kitaraka za Jimbo la Manyoni Magharibi hazina umeme kabisa jambo ambalo linakwamisha jitihada za wanawake na vijana kujikomboa kiuchumi.

Je, Serikali ina mkakati gani wa haraka wa kupeleka umeme katika umeme vijiji hivyo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa vijiji vya Kinyamwenda, Itaja na Ngimu vya Jimbo la Singida Kaskazini ambavyo vilikuwa katika mpango wa mradi wa backbone unaoanzia Singida, Arusha hadi Namanga havina umeme kabisa.

Je Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha vijiji hivi vinakuwa na umeme? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Aysharose Mattembe kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa kuwa amekuwa mstari mbele sana kufuatilia upelekaji wa umeme katika Mkoa wote wa Singida na tumekuwa mara kwa mara tukijadiliana na kuhakikishia kwamba hakika tutafikisha umeme katika maeneo yote ya Kinyamwenda kama alivyosema, Kitalaka na kata nyingine ambazo ziko katika maeneo yake.

Mheshimiwa Spika, kama tulivyosema mkandarasi anayetarajiwa kupeleka umeme katika Mkoa wetu wa Singida kwenye Wilaya yetu ya Manyoni ataanza kazi mwezi unaokuja na tutahakikisha kwamba vijiji hivyo vyote 14 ambavyo vilikuwa vimebakia bila kupelekewa umeme vinapata umeme.

Mheshimiwa Spika, lakini katika swali la pili hayo maeneo mengine ambaye ameyasema yamechukuliwa na mkandarasi ambaye anapeleka umeme kutoka Iringa kupita Dodoma, Singida kwenda Arusha kwenda mpaka Namanga na viko katika scope yake na kazi yake inatakiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi wa saba.

Mheshimiwa Spika, tunafahamu kwamba tayari vifaa vya kufanya kazi hiyo vipo site kwa maana ya nguzo, waya na transfoma na tutahakikisha kwamba tunasimama naye ili katika muda aliopewa aweze kukamilisha kazi hiyo ili wananchi wote wa Singida waweze kupata umeme kwa ajili ya maendeleo katika maeneo yao, ahsante.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kuuliza swali moja la nyongeza; ni lini Serikali itapeleka umeme kwa vijiji 28 ambavyo viko katika Jimbo la Handeni Mjini havijapata umeme mpaka sasa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kwagilwa Mbunge wa Handeni Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia na yeye kwa kuendelea kufuatilia upelekaji wa umeme katika maeneo yake. Jimbo la Handeni Mjini halina tofauti na Jimbo la Bukoba Mjini ambao ni maeneo ambayo hayakuwa yananufaika na Mradi wa REA, lakini sisi tumeweka katika mradi wa peri urban ambao tunatarajia kuuanza mwezi wa tisa na hivyo maeneo yote ya mijini ambayo pengine bado yanaonekana yana nature ya vijiji; Jimbo la Bukoba Mjini, Handeni Mjini na maeneo mengine yakiwepo yatapelekewa umeme kuanzia mwezi wa tisa kupitia mradi wetu wa peri urban ikiwa ni pamoja na Ilemela, Mwanza na maeneo kama ya Geita ambayo yako mjini, lakini yana hadhi ambayo ya kijijini. Nashukuru.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana; kwanza nikupongeze wewe kwa kazi nzuri ambayo unaifanya kuelekea kuhitimisha Bunge letu la Bajeti.

Mheshimiwa Spika, naomba niulize swali la nyongeza, lakini kabla ya kuuliza kwanza niipongeze Serikali na Wizara ya Nishati kwa kazi nzuri na kubwa inayoifanya kwa sababu wakati Wizara ya Nishati inatoa taarifa yake ilisema itamalizia umeme REA Awamu ya Tatu vijiji vyote vya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, na ninataka niwahakikishie kwamba katika Jimbo langu la Mchinga wataalam wako kazini tangu tarehe 16 mwezi huu wa Juni wakiwa na mkandarasi anayeitwa Nakuroi Investment Company Limited wanafanya kazi nzuri sana. Vijiji vyote kama Kijiji cha Kiwawa, Mputwa, Ruvu na Mtamba, Luchemi, Lihimilo Mnyangala, Namkongo, Makangala na Luhoma; hivi vijiji vyote vimeshafikiwa, isipokuwa kuna vijiji viwili tu ambavyo vimesahaulika. (Makofi)

Nakuomba sana na ninaiomba Serikali katika awamu ile ya tatu wamalizie hivyo vijiji viwili ambavyo ni Kijiji cha Dimba na Kijiji cha Kitohave. Ahsante sana Mheshimiwa Waziri.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nipende kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, Mbunge wa Mchinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa shukrani kwa niaba ya Wizara, lakini na Serikali kwa Mheshimiwa Mbunge kuona kwamba Serikali kwa ujumla yake chini ya uongozi wa Mheshimiwa wa Mama Samia Suluhu Hassan imeamua kuhakikisha kwamba inawafikishia umeme Watanzania wote mahala walipo, na kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili kuhakikisha vijiji vyote ambavyo amekuwa amepelekewa umeme vinapelekewa.

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema Mheshimiwa Mbunge kwa niaba ya Wabunge wengine tunafurahi kwamba sasa wakandarasi katika maeneo yetu mengi tayari wako site, kazi tayari zimeanza za kufanya survey na kuhakiki vijiji ambavyo vimechukuliwa na vitapewa umeme.

Mheshimiwa Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wale ambao katika maeneo yao hawajawaona wakandarasi au wameendelea kupata changamoto ya mawasiliano na wakandarasi hao basi tuwasiliane ili tuweze kuhakikisha kwamba tunasimamiana ili katika muda ambao tumewahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwamba tutapeleka umeme katika maeneo yetu, tuweze kufikisha umeme kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, juzi Mheshimiwa Waziri alisema kwamba vilikuwa vimebaki vijiji kama 680 ambavyo havikuwa vimeingia kwenye ile awamu yetu, lakini tayari maelekezo yametolewa na vijiji vyote vilivyoko katika maeneo yetu vimechukuliwa na vitafanyiwa kazi katika Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili bila kuacha hata kijiji kimoja.

Mheshimiwa Spika, hii ni commitment ya Serikali kwamba ifikapo Disemba, 2022 vijiji vyote ambavyo viko katika maeneo yetu vitakuwa vimepata umeme na kuhakikisha kwamba wananchi wote wanaendelea kufarijika na huduma ya umeme kwa ajili ya maendeleo katika maeneo yetu nashukuru sana.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba niulize mswali mawili madogo ya nyongeza.

Swali la kwanza, kuna baadhi ya vijiji ambavyo vimeachwa katika huu mkakati ambao sasa unaenda kutekelezeka wa vijiji hivi 29, mathalani Vijiji vya Sagara, Itaja, Kinyamwenda, Mwighanji, Itamka, Endesh, Sefunga, Namrama havijaonekana.

Sasa Serikali inampangao gani kuhakikisha vile vijiji vyote vilivyoachwa vionekane sasa katika ramani ili navyo vinufaike na mradi huu?

Mheshimiwa Spika, katika maeneo ambayo yameshapatiwa umeme, kuna vitongoji vikubwa vyenye hadhi ya kijiji na taasisi za umma kama vile shule na zahanati, lakini umeme umeishia pale tu center, na hapo hapo kuna maeneo ambayo tayari walishafanya na wiring waliagizwa wafanye wiring na umeme haujafika.

Sasa ningependa kujua Serikali ina mpango gani kuhakikisha maeneo yale ambayo ni makubwa yana hadhi ya kijiji nayo yapatiwe umeme? Naomba kuwasilisha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abeid, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna vijiji ambavyo vilionekana vimebaki katika kuchukuliwa kwa awamu ya tatu mzunguko wa pili wa REA, na amevitaja vijiji sita, vijiji vitatu vya Endesh kinyamwenda na Endesh nyengine viko katika mradi wa backbone ambao unatoka Iringa kwenda kupeleka umeme mpaka Namanga, kwa hiyo ule mradi mkubwa umechukua vijiji vitatu ambavyo tutavipatia umeme. Mkoa wa Singida una vijiji saba ambavyo tumeviweka kwenye ule mradi, vijiji vitatu viko Singida Kaskazini na vitaingia kwenye huo mradi na vitachukuliwa na vitapatiwa umeme kufikia mwishoni mwa mwezi Julai.

Mheshimiwa Spika, vijiji vyengine vitatu vinavyobakia vimechukuliwa katika hivyo 26; kama tulivyosema hapo awali kwamba kuna maeneo ambayo yalikuwa yamebaki na takriban vijiji 680 vyote yameingizwa kwenye REA Awamu ya Tatu mzinguko wa pili, na yote yatafanyiwa kazi kwa pamoja ili inapofika Disemba 2022 vijiji vyote Tanzania Bara viwe vimepata umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili ni kweli kwamba kuna maeneo yetu ya vitongoji bado hayajapata umeme, na kama ambayo tunavyokuwa tukisema maendeleo ni hatua taratibu tunawafikia, tulianza kwenye vijiji na tunamaliza Disemba mwakani, kwenye vitongoji tunaendelea kufika na speed yetu ni nzuri na tunamini kwamba muda kabla haujawa mrefu sana, kila kitongoji kitakuwa kimepatiwa umeme.

Mheshimiwa Spika, kwenye vitongoji TANESCO ni jukumu lao la kila siku wanaendelea kupeleke kwenye maeneo yetu, na REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unapoingia kijijini utafika pia kwenye vitongoji na pia miradi yetu mingine ikiwemo densification ambayo tunatarajia ianze mwezi wa 10 itachukua walau sehemu ya vitongoji ili zoezi
hilo la kupeleka umeme kwenye vitongoji liweze kukamilika na wananchi waweze kupata umeme, ahsante.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Kwa kuwa dhamira ya Serikali ni kupeleka umeme katika vijiji vyote katika nchi ya Tanzania nzima ikiwemo na vitongoji, lakini kuna changamoto katika Wilaya ya Manyoni feeder ya Manyoni kutoka Singida ambayo inahusisha Wilaya ya Ikungi, Wilaya ya Manyoni na Halmashauri ya Itigi, umeme wake una katikakatika mara kwa mara, na ipo dhamira njema ya Serikali ya kujenga vituo vya kupozea umeme katika Mkoa wa Singida vipo vitatu ikiwepo Manyoni, Mitundu katika Jimbo langu na Iramba; je, ni lini ujenzi wa vituo hivi unaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa mgunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba yapo baadhi ya maeneo ambayo umeme wake unakuwa haufiki vizuri kwa sababu ya laini kuwa ni ndefu, lakini Mkoa wetu wa Singida ni mkoa mmojawapo wenye kituo kikubwa sana cha kupoza umeme pale mjini, na umeme unatokea pale kuelekea maeneo ya jirani, na tunao umeme wa kutosha kuweza kuhudumia maeneo yote. Ni kweli tunatarajia kuweka vituo vyengine vya kupoza umeme katika maeneo yetu ya Singida, mchakato wa kutafuta wazabuni na maeneo sahihi ya kuweka unaendelea, kabla ya mwaka huu haujaisha Waheshimiwa Wabunge wataona maendeleo katika maeneo yao na ikiwemo kwenye Jimbo lake ambapo tunatarajia kuweka kituo cha kupoza umeme kwa ajili ya kuweza kusambaza umeme kwa karibu zaidi katika maeneo yake.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na changamoto kubwa katika Mkoa wa Manyara ya upandishwaji wa gharama za umeme kutoka kwa wananchi kutoka unit zero mpaka kupelekwa unit one. Changamoto hiyo imetokea wananchi walikuwa wanalipa umeme wa shilingi 5,000 wanapata unit 41, na kwa sasa hivi wananchi wakinunua umeme shilingi 5,000 wanapata umeme unit 14; na Wilaya zilizoathirika ni Wilaya za Hanang, Mbulu, Babati, Simanjiro kwa ujumla wake mkoa mzima wa Manyara.

Nini kauli ya Serikali juu ya kuwapa umeme kwa bei ya kawaida wananchi wa Manyara ili waweze kujiinua kiuchumi na wasilale giza? Ahsante.
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, Mbunge wa Taifa Vijana kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba gharama za umeme ziko juu hata hizo zinazosemwa ni ndogo sisi bado tunaziona ziko juu. Nia ya Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha umeme unakuwa wa gharama nafuu na kila mmoja anaweza kuupata kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi pia na ya kijamii.

Mheshimiwa Spika, tariff tunazozitumia sasa zilitengenezwa mwaka 2016 na EWURA ndiyo msimamizi wa gharama za utoaji wa umeme kwa watu mbalimbali. Sasa naomba nieleze kinachotokea; zile tariff, ile kanuni ya gharama inasema mtu anayetumia unit sifuri mpaka unit 75 atakuwa-charged shilingi 100 kwa unit moja, yule anayetumia zaidi ya unit 75 na kuendelea gharama zake ni shilingi 200 hadi 350 kulingana na yuko kwenye tariff I, tariff II au tariff III.

Sasa kuna kifungu kwenye kanuni ile kiliwekwa kwamba wananchi wote wanaotumia umeme wakiwa maeneo ya vijijini wapate gharama hiyo ya unit moja shilingi moja na wanaozidi 75 waendelee kwingine. Wale ambao sio wa maeneo ya vijijini hawapati nafuu ya punguzo hilo la gharama.

Mheshimiwa Spika, lakini baada ya kuona kwamba kanuni hizo zilitengenezwa kipindi ambacho kulikuwa na shida sana ya upatikanaji wa umeme wa gharama nafuu kwa maana ya kutumia mafuta mazito na mitambo mingine, lakini sasa tuanzalisha umeme kutoka kwenye maji ambako ni nafuu, tunayo gesi yetu ya kutosha kabisa kwa ajili ya kuzalisha umeme.

Mheshimiwa Spika, tumekubaliana na wenzetu wa TANESCO, wakae chini, wa-review hizo gharama za kuuza umeme ili tuweze kupata umeme mwingi zaidi na tukauuza kwa gharama ndogo.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Asia pamoja na Waheshimiwa wengine watuvumilie kidogo, tuko katika mapitio mazuri kabisa ya kushusha gharama za kuuza umeme na kila mmoja atapata gharama hiyo ya umeme nzuri kabisa kwa ajili ya maendeleo kwenye maeneo yetu ya mijini na maeneo ya vijijini ili ile nia ya uwekezaji ambayo Mheshimiwa Rais anaitaka kwa Watanzania wote iweze kufikiwa kwa kila mmoja. Ahsante. (Makofi)
MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru; miongoni mwa ahadi za uendelezaji wa nishati ya gesi ni pamoja na ujenzi wa kiwanda kikubwa cha mbolea. Naomba nipate ufafanuzi wa Serikali ni lini kiwanda hicho kitajengwa katika mkoa wa Mtwara?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; sisi watu wa Mtwara kila siku tunauliza gesi kwa sababu hatuoni ile michakato ambayo tulikuwa tunaiona pale nyuma. Sasa hivi Mtwara habari ya gesi ni kama haipo, kama imelala. Hata Ripoti ya CAG ukiisoma inaeleza kwamba matumizi ya gesi bado yako chini.

Sasa nataka tu kujua kauli ya Serikali; ni nini hasa inafanya ili sisi watu wa Mtwara turidhike kwamba ile gesi iliyogundulika Mtwara inafanya lile ambalo limekusudiwa na kuinua uchumi wa watu wa Mtwara na Taifa kwa ujumla? Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali ilianza majadiliano na wawekezaji wa viwanda vya kutengeneza mbolea kwa kutumia gesi almaarufu kama petrochemicals. Hiyo gesi ndiyo malighafi kubwa katika utengenezaji wa hizo mbolea na vitu vya namna hiyo. Sasa kilichotokea ni kwamba biashara ile ilionekana haikuwa ya kutusaidia na kutufaa kwa kipindi hicho kwa sababu wakati duniani wanataka kununua kwa dola tatu sisi wa kwetu walikuwa ana bei ya chini kabisa ambayo ilionekana haitakuwa faida kwa Taifa.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa sasa tumefungua upya milango ya majadiliano na wawekezaji mbalimbali wanaotaka kuwekeza katika viwanda kama hivyo akiwemo mwekezaji mkubwa wa Dangote naye ameonesha nia na bado tunaendelea kupokea maombi na majadiliano mbalimbali yanafanyika kuhakikisha kwamba sasa tunaweza kutumia gesi kutengeneza viwanda vya malighafi mbalimbali kama hivyo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunakoelekea ni kuzuri na viwanda vya petrochemicals na vingine vitakuja. Gesi tutaitoa huko iliko na kuitumia kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili; ni kweli kwamba kwa muda mrefu kidogo pameonekana kama pamelala kwamba hakuna kilichokuwa kinaendelea. Kimsingi kilichokuwa kinaendelea ni kikubwa kuzidi kilichokuwa kinaonekana. Tunayo mikataba inayoitwa Production Sharing Agreement (PSA) ni mikataba ambayo inaingiwa kati ya Serikali na wale wawekezaji wanaokuja kuwekeza katika maeneo yetu ya gesi. Tukikubaliana tutazalishaje, tutagawana vipi na tutatumia vipi.

Mheshimiwa Spika, sasa majadiliano hayo yamechukua muda mrefu na marekebisho na mapitio ya mikataba hiyo imechukua muda mrefu, lakini sasa yamekamilika na tayari Serikali imetoa maelekezo na sasa kinachofanyika ile Kamati ya Serikali ya ku-negotiate mikataba imerudi tena kazini na tunatarajia mwezi wa 10 itakuwa imekamilisha kazi yake ya ku-negotiate sasa mikataba ya matumizi na unufaikaji wa gesi na tunatarajia kuanzia mwezi wa 11 basi mambo yataanza kuwa vizuri. Gesi hii tunayoitoa na kuitumia sasa itaongezeka zaidi kwa ajili ya manufaa ya nchi kwa ujumla. (Makofi)
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nataka kuulizia kwamba mradi wa LNG wa Lindi mazungumzo yake yamechukua muda mrefu sana; ni zaidi ya miaka saba na hata wawekezaji wengine ambao wanataka kuwekeza kwenye shughuli za petrochemicals wameshakata tamaa. Ni nini sasa kauli ya Serikali kwamba mazungumzo hayo yanatarajiwa kukamilika?
NAIBU WAZIRI NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Chikota kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kusema majadiliano yalisimama ili kupisha mapitio ya mikataba ya uzalishaji wa gesi na sasa majadiliano yameanza tena kuanzia mwezi wa nne na tunatarajia mwezi wa 10 majadiliano hayo yatakuwa yamekamilika na mwekezaji anaweza akaanza kuwekeza muda wowote baada ya hapo.

Mheshimiwa Spika, LNG ikitolewa kule tunakwenda mbele zaidi na kuisambaza katika maeneo mengine. Tutajenga vituo vitano vya ku-compress gesi na kuweza kuiuza kwa wananchi Dodoma ikiwa ni mojawapo.

Kwa hiyo, tutaweza kupata gesi asilia tukiwa hapa hapa Dodoma baada ya kukamilisha majadiliano na kuanza kujenga vituo vingine ambapo katika bajeti ya wenzetu wa TPDC imetengwa takribani shilingi bilioni 28 kwa ajili ya ujenzi wa vituo hivyo vitano katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwishoni mwa mwaka huu wataanza kufurahia matumizi ya gesi kwa sehemu kubwa ya nchi yetu.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru tena kwa kunipa nafasi. Kwanza niseme naishukuru sana Serikali na kuipongeza kwa kazi nzuri ambayo inafanya kwa kuhakikisha kwamba inawasha umeme kwa vijiji vyote na vitongoji nchi nzima. Hata hivyo, hivi karibuni tulipata orodha ya wakandarasi ambao wamekuja kwa ajili ya kufanya kazi ya kumalizia zoezi la kuwasha umeme REA III.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule Arusha Mkoani amekuja kandarasi mmoja tu na kule Longido, nakuwa na mashaka kwamba ahadi ya Serikali kwamba mwaka kesho watakuwa wametimiza ahadi yao ya vijiji vyote nchi nzima kuwa vimeshapata umeme; nakuwa na mashaka kwamba tutaweza kufanikisha hilo zoezi. Swali langu, je, wana mpango gani wa kuhakikisha kwamba wanaongeza idadi ya wakandarasi ili hiyo kazi na ahadi ya Serikali iwe ya kweli? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru kwa kutambua juhudi za Serikali za kuendelea kuwahudumia watanzania kwa kuwapelekea umeme katika maeneo yao na ni commitment ya Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwamba kufikia Disemba, 2022, tutakuwa tumekamilisha upelekaji wa umeme katika maeneo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli wiki kama mbili zilizopita Mradi wa REA III, round II, ulizinduliwa rasmi na Mheshimiwa Waziri katika eneo la Longido na mkandarasi anayefanya kazi katika Mkoa wetu wa Arusha anaitwa SAGEMCOM na yuko kazini tayari na alikuwa amepewa maeneo matatu ya Longido, Karatu na Monduli.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na upana wa Mkoa wa Arusha, Wizara imeona ni vema kuongeza mkandarasi mwingine, aende akafanye kazi katika Jimbo la Arumeru Mashariki, Mgharibi lakini pia na Ngorongoro. Kabla ya mwezi Julai haujaisha mkandarasi atakuwa ameripoti kazini kwa ajili ya kuendelea kufanya kazi ili ile ahadi iliyotolewa na Serikali ya kufikisha umeme kwa wananchi wote ifikapo Disemba mwakani iwe imekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie nafasi hii kuwaomba Waheshimiwa Wabunge kwa sababu baada ya hapa tunatawanyika kwenda kwenye maeneo yetu basi wakawe mkono wa kwanza kabisa wa kushirikiana na
wakandarasi kutimiza azma ya kupeleka umeme kwa wananchi kwa kuwasimamia kwa karibu na kuwa pamoja na sisi ili kuweza kufikisha hiyo ahadi. Nashukuru.
MHE. DANIEL A. TLEMAI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Katika Wilaya ya Karatu kuna Mji Mdogo wa Karatu, sasa huu Mradi wa REA umelenga sana kwenye vijiji na pale Mji wa Karatu wanasema ni mjini lakini ni bado vijijini sasa ni lini Serikali ina mpango gani katika ile miji midogo ambayo umeme huu wa REA haujapelekwa ili kuwasaidia wananchi wakiwemo wa Jimbo la Karatu wa Mji wa Karatu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daniel Awack, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli upelekaji wa umeme unaofanywa na Serikali uko katika picha na maeneo tofautitofauti; ziko hizo tunazoziita REA ambapo tumekuwa na awamu kadhaa, lakini iko miradi ya densification, inapeleka umeme kwenye vitongoji, lakini hiko miradi tunaita peri-urban.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya peri urban inapeleka umeme kwenye maeneo ya miji lakini ambayo bado yana asili ya vijiji, Jimbo la Bukoba Mjini likiwemo na kwa Karatu ikiwemo, maeneo ya Mwanza yakiwemo, Geita ikiwemo, tutahakikisha kwamba kufikia mwezi Februari tumeanzisha huo mradi wa peri-urban unaoweza kupeleka umeme kwenye maeneo ambayo ni ya mijini lakini bado yana asili ya vijiji ili na sisi pia tuweze kunufaika na umeme huo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwanza, nimpongeze Naibu Waziri kwa kazi anayofanya na Waziri mwenyewe kwenye Wizara hii. Lakini tatizo lililoko sasa REA inapokwenda kwenye kupeleka umeme vijijini zinapelekwa nguzo 20 tu na kwa sababu ni vijijini, nyumba ziko mbalimbali inatokea nyumba 10 tu zinapata umeme vijijini. Je, REA mnaonaje kwa nini msiongeze nguzo ili nyumba nyingi zikapata nguzo kuliko kupata nguzo hizo 20? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Waziri amekuwa akitoa taarifa ya wateja wanaotumia unit chini ya 70 kuuziwa unit kwa shilingi 100. Lakini sasa wateja hawa wanauziwa unit kwa shilingi 300. Je, Serikali ina mpango gani wa kutoa taarifa humu ili wananchi hawa wakajua nini hasa, umeme unatakiwa kulipiwa kwa hawa wateja wanaofikisha unit chini ya 70? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya ngongeza ya Mheshimiwa Flatei kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumshukuru kwa pongezi alizozitoa kwa Wizara na kweli tunaendelea kujitahidi kwa maelekezo ya Serikali kuhakikisha tunatimiza maelekezo tunayopewa. Lakini nimpongeze kwa kufuatilia maeneo kwenye Jimbo lake na mimi nilienda kuzindua umeme na mambo yanakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, na nimuhakikishie kwamba nguzo 20 ni kwa wateja wa awali. Naomba uniruhusu nichukue nafasi hii kuwaeleza Waheshimiwa Wabunge wote kwamba, tunapoendelea na mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili karibia kila eneo tumetoa kwa kuanzia nguzo 20. Lakini ni wateja tunawaita wateja wa awali sio kwamba ndio tumemaliza zoezi, kadri muda unavyozidi kuendelea TANESCO wataendelea kupeleka umeme katika maeneo hayo. Lakini pia REA wenyewe wataendelea kuongeza wigo wa kazi wanayoifanya kuhakikisha kwamba sasa watu wengi zaidi wanapata umeme katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la pili kuhusiana na gharama za umeme. Kabla sijajibu kwanza nipende kutoa shukurani zetu kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Sita, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kwa kuamua kuwapenda watanzania na kuwafikishia huduma ya umeme kwa gharama nafuu. Kwanza nguzo haziuzwi, mita haziuzwi, nyaya haziuzwi na connection ya umeme ni shilingi 27,000/= tu na hayo ndio maelekezo ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo la umeme mwaka 2016 zilitengenezwa Kanuni kulingana na mazingira tuliyokuwa nayo, ambazo zilikuwa zinasema waunganishiwaji wote wa umeme na watumiaji wa umeme wa maeneo ya vijijini watauziwa unit 1 kwa shilingi 100 endapo matumizi hayazidi unit 75 kwa mwezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini maeneo ya Mijini hayakuwa yanahusika na utaratibu huu. Lakini baada ya kufikisha miundombinu mingi zaidi kwenye maeneo hata ya mjini tangu Disemba mwaka jana, Serikali imeelekeza popote pale ulipo ili mradi unatumia unit zisizozidi 75 gharama ya unit 1 itakuwa ni shilingi 100/=. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba unipe nafasi ya kuwaelekeza Mameneja wote wa TANESCO nchi nzima, kukamilisha utaratibu ambao Serikali imeelekeza kupitia Wizara ya Nishati. Kuhakikisha watu wote wanaotumia umeme chini ya unit 75 kwa mwezi, kupata gharama kwa shilingi 9,150 ambayo ni unit moja ni shilingi 100. Na zoezi hili lilianza tangu mwezi wa saba. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri swali lake ni kwamba, Serikali haioni namna ambavyo wale wanatakiwa kuendelea kuuziwa? Maana yake umeme umepanda bei kwa swali la Mheshimiwa Mbunge ni kwamba umeme sasa hauuzwi unit shilingi 100 umepanda. Sasa unampa maelekezo nani wewe ndio tunakusikiliza hapa, kwa nini umepanda yaani ndio swali lake. Kwa nini wasiendelee kuuziwa vile vile ile bei iliyokuwepo? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutoa ufafanuzi. Umeme haujapanda bei, kwa siku za hivi karibuni kumekuwa kuna utaratibu mpya wa kukusanya kodi ya majengo kupitia kwenye LUKU. Tunaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuwaelimisha kwamba hizo sio gharama za umeme bali ni conduit tu ya kupitisha hizi gharama za upande wa pili.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo la umeme, kilichotokea ni kwamba, utaratibu wa kuwaweka watu kwenye gharama ndogo ulikuwa haujafanyika. Kwa hiyo, watu waliwekwa kwenye gharama kubwa kwa maana ya kwamba waliwekwa kwenye viwango sahihi kwa mujibu wa Kanuni zilizokuwepo mwaka 2016. Sasa kuanzia Disemba mwaka jana Kanuni zilirekebishwa na utekelezaji unaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, maelekezo ya Serikali ni kwamba, wale wote ambao walikuwa wamepelekwa kwenye tunazoziita Tariff 1, Tariff 2 na Tariff 3, lakini gharama zao hazizidi unit 75 kwa mwezi warudishwe kwenye tunayoita D1 ambayo ni domestic one ambayo unit ni shilingi 100.

NAIBU SPIKA: Sasa ngoja, sasa hapo umeshajibu. Wewe kaa. Maana yake ni kwamba bei inatakiwa kuwa ni ile ile sasa wewe wasiliana na watu wako wa TANESCO huko, wasiwauzie bei zaidi ya ile iliyokuwepo mwanzo ndio jibu lako hapo. (Makofi)

Kwa hiyo, Mheshimiwa kama utaendelea kupata changamoto huko Mbulu Vijijini bila shaka utampigia simu Mheshimiwa Naibu Waziri, ili awaeleze hao wa huko Mbulu Vijijini waliopandisha hiyo bei. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri wa Nishati na ni kweli mkandarasi yupo site anaendelea na kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa vijiji 11 vya awali vilivyopata umeme awamu ya kwanza, ya pili na ya tatu umeme ule ulipita barabarani bila kupita mitaa yote katika vijiji hivyo kama ville ilivyo Azimio, Chiwana, Mbesa pale Tuwemacho na Ligoma. Ni lini sasa Serikali itaona haja ya kupeleka kuanza mradi wa ujazilizi katika vijiji hivyo ili vitongoji vyote vilivyopo kwenye vijiji hivyo vipate umeme.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza ya Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba plan na maelekezo ya Serikali ni kuhakikisha kwamba vijiji vyote 12,268 vinapata umeme ifikapo Desemba mwakani na hilo sisi kwa kutekeleza maelekezo ya Serikali tunaiahidi umma kwamba tutakamilisha maelekezo hayo kwa kadiri ilivyoelekezwa na ilivyoazimiwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la vitongoji, upelekaji wa umeme kwenye eneo la vitongoji ni zoezi endelevu ambapo wenzetu wa TANESCO wanaendelea kupeleka umeme katika maeneo hayo lakini pia vipo vitongoji vingi ambavyo vitaguswa na Mradi huu wa REA III round two. Lakini specifically upo mradi wa vitongoji ambao ni wa densification yaani umeme jazilizi ambao tunatarajia uanze mwenzi wa 10 mwishoni ambao utahusika pia katika kupeleka umeme kwenye vitongoji alivyovitaja katika Jimbo la Tunduru Kusini. Nashukuru.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, changamoto ambayo ipo kwa Mheshimiwa Mpakate kuhusu umeme wa REA pia ipo Makete ambapo mkandarasi aliyemaliza kutekeleza mradi wake yeye anasema amemaliza lakini bado tuna changamoto ya kwamba kuna Vijiji kama Mago, Mbela na Kinyika ambako tuna zaidi ya nyumba 1,000 ambazo wananchi wameshasuka umeme toka 2019 lakini hadi ninavyozungumza muda huu wananchi hao hawajaingiziwa umeme kwa sababu ya kwamba mita na nguzo zimeisha.

Je, ni ipi kauli ya Serikali kwa huyu Mkandarasi wa REA ambaye hajakamilisha kazi yake ipasavyo ndani ya Jimbo la Makete na wananchi wangu wanaendelea kuteseka? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Festo Sanga, Mbunge wa Makete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunapompatia mkandarasi kazi, tunampa wigo wa kufanya kazi ambayo tunaita ni wateja wa awali. Na kwa wakandarasi wa REA III Round One wako wakandarasi kama wanne ambao walikuwa hawajakamilisha kazi zao ambao tumewaelekeza ifikapo mwishoni mwa mwezi wa 10 wawe wamekamilisha kazi zote. Hivyo, tunatarajia kuanzia mwezi wa 11 hakutakuwa kuna mkandarasi ambaye alikuwa anafanya kazi tofauti na REA III Round Two ambaye atakuwa bado yupo kazini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baaada ya hapa nitafuatilia na kujua hivyo vijiji vilivyobaki ni vingapi na avikamilishe kwa sababu kwenye REA III Round Two hatutaacha kijiji hata kimoja ambacho hakitapata umeme ifikapo Desemba mwakani. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi. Pamoja na majibu mazuri sana ya Serikali, lakini yapo maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Mkoa wa Singida eneo ambalo linaathirika sana na ukatikaji wa umeme ni eneo la Itigi, lakini na Manyoni wao wanaita feeder ya Manyoni na kila Jumamosi au Jumapili ya wiki lazima umeme ukatike. Sasa je, ni lini zoezi hili litakoma kukatwa katwa umeme katika Halmashauri ya Itigi?

Mheshimiwa Spika lakini pili tunachangamoto ambayo imetokea sasa wakati wenzetu wanaendelea na wakandarasi wa REA nchi nzima katika wilaya ya Manyoni hakuna mkandarasi. je, ni nini tatizo na ni lini mkandarasi wa REA III atapatikana katika Halmashauri za Manyoni na Itigi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Massare kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na swali la pili la Mkandarasi wa REA. Ni kweli kwamba Serikali ilitangaza kazi za kutengeneza umeme wa vijijini na maeneo mengi yakawa yamepata wakandarasi, lakini maeneo Matano yalibaki bila kupata wakandarasi ikiwemo Singida kwa maeneo ya Itigi na Manyoni ni mojawapo.

Mheshimiwa Spika, napenda kutoa taarifa kwenye Bunge lako Tukufu kwamba Ijumaa ya wiki iliyopita, Mkandarasi anayeitwa TungTang amesaini mkataba wa kupeleka umeme katika Wilaya zetu za Itigi na Manyoni na
tumemwambia aripoti kazini Jumatatu ijayo wakati sisi ofisini Serikali ikiwa inaendelea kukamilisha utaratibu wa malipo ya awali.

Mheshimiwa Spika, nitumie nafasi hii kusema kwamba, lot ya Singida iko pamoja na lot ya Shinyanga, Tanga na Arusha. Wakandarasi wote hawa tunatarajia waanze kuripoti katika maeneo yao ya kazi kuanzia Jumatatu ya wiki ijayo.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la kukatikakatika kwa umeme, nianze kwa kusema kwamba tunaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa jinsi ambavyo inaonekana wazi kabisa kwamba kuna mabadiliko makubwa ambayo yamefanyika katika Wizara ya Nishati, lakini katika Shirika letu la TANESCO na tunatarajia kabisa kwamba katika kipindi kifupi kijacho wenzetu ambao wamepewa dhamana sasa TANESCO wataenda kukidhi yale mahitaji ambayo Watanzania wanayatarajia.

Mheshimiwa Spika, siyo hilo tu, bajeti ya TANESCO sasa imewekewa mechanism ya kuhakikisha inaongezeka kwa kuziba ile mianya iliyokuwa ikiachia mapato yavuje ili kuweza kupata nguvu zaidi sasa ya kuimarisha maeneo hayo ya kukatika kwa umeme. Kukatika kwa umeme kunasababishwa na sababu nyingi nyingi, lakini zile ambazo ziko ndani ya uwezo wetu tunahakikisha kwamba tunazifanyia kazi ili tatizo hilo liweze kwisha, siyo kwa Itigi na Manyoni peke yake, lakini kwa nchi nzima. Naomba kuwasilisha.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika ahsante. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, pia Halmashauri ya Mji wa Ifakara Jimbo la Kilombero imekuwa ikikosa umeme kila Jumanne na Alhamis; na tunamradi mkubwa sana wa Serikali wa zaidi ya shilingi bilioni 20 wa kituo cha kukuzia umeme. Ujenzi huo wa mradi unasuasua kwa muda mrefu sana: -

Je, Naibu Waziri atakuwa tayari kutembelea pale kutazama changamoto za kusuasua za mradi ule?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako nipo tayari kwenda kuangalia changamoto hizo, lakini niseme kwamba kama anasema ni Jumanne na Alhamis, basi nitafanya mawasiliano na wenzangu tufahamu shida ni nini?

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie Watanzania kwamba hatuna mgao kwa nchi yetu ya Tanzania kwa sasa. Tunao umeme ambao unatosheleza mahitaji tuliyokuwa nayo kwa kile kiasi tunachoweza kupeleka, lakini tutaenda kuangalia tatizo ni nini ili tuweze kulitatua.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Spika ahsante, kwa kuwa ni swali la msingi liliulizia bei ya umeme, nami niulize ni lini TANESCO itatausha bei ya umeme inayouza ZECO?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ali King kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, TANESCO kwa maana ya Shirika la Umeme Tanzania imekuwa na mkataba na Shirika la ZECO kwa maana ya Shirika la Umeme la Zanzibar kwenye kuuziana umeme. Tumekuwa na bei ambazo zinatofautiana; na tumekuwa tuna majadiliano kwa muda mrefu katika eneo hili na jambo hili likapelekwa mpaka kwenye kamati zetu zinazoshughulikia maswali ya na Muungano.

Mheshimiwa Spika, issue kubwa ilikiwa ni habari ya bei. TANESCO walikuwa wanaona wakiuza umeme kwa shilingi 130/= ambayo wenzetu wa ZECO wanaihitaji hawataweza kwa sababu itakuwa ni hasara. ZECO wanasema sisi tukiwauzia kwa shilingi 156/= ambayo tunaona ni gharama za chini za kuzalisha, hatutaweza kufanikiwa kwa sababu ZECO wanasema hiyo kwao ni gharama kubwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kumekuwa na mazungumzo yanayoendelea na suala hilo limepelekwa katika Kamati ile inayoshughulikia masuala ya Muungano na tunasubiria maelekezo ya Serikali ili kuona namna gani tunaweza kusaidia mashirika haya mawili yaweze kuendelea kushirikiana na kukamilisha upelekaji wa umeme kwa gharama nafuu kwa wenzetu wa Zanzibar. (Makofi)
MHE. TASKA R. MBOGO: Mheshimiwa Spika ahsante, kwa kunipa nafasi kwa kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri sana ya Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusu umeme ninayo maswali mawili ya nyongeza kwa Mkoa wa Katavi.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza wananchi wa Mkoa wa Katavi wanahitaji umeme wa gridi kwa haraka ili waweze kujenga viwanda, lakini pia ili waweze kufanya biashara zao mbali mbali zinazotumia umeme. Kumekuwepo na kusuasua kwa mradi huu wa umeme wa gridi na ujenzi wake unakwenda taratibu kwa sababu ya ufinyu wa pesa zainazotolewa Serikalini kwenda TANESCO: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuongeza bajeti ya TANESCO ili waweze kujenga miundombinu ya umeme kwa Mkoani Katavi? (Makofi)

Swali la pili; umeme uliopo sasa hivi Mkoa wa Katavi hautoshelezi kwa sababu kumeuwa na usambazaji wa umeme wa REA, hivyo watumiaji wa umeme ni wengi mkoani Katavi. Swali langu na ombi langu kwa Serikali: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutupunguzia muda wa ukamilishaji wa ujenzi wa umeme wa gridi badala ya kuwa 2023 uwe 2022? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita imejipambanua kuwa na uwezo wa kutekeleza miradi ambayo imeianzisha na ile ambayo imeikuta ikiwa inaendelea, nasi tuna uhakika kwamba fedha iliyopo TANESCO itaendelea kutosha na pale ambapo watapungukiwa Serikali itaongeza. Katika bajeti ambayo Bunge lako limepitisha jusi, takribani shilingi bilioni 35 zilitengwa kwa ajili ya kuendelea na hii kazi ya ujenzi wa hiyo njia ya msongo wa kilovolti 132 kutoka Tabora kwenda Mpanda.

Mheshimiwa Spika, tunaamini fedha hizo zitatosha na kwa kadri itakavyohitajika kutoka kwa wataalamu basi Serikali itaongeza pesa hizo kwa sababu inazo.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili, kwa kuwa wenzetu wa Katavi hawajafikiwa na gridi; na gridi kwa mujibu wa ratiba ya TANESCO iliyowekwa kwa mchanganuo ule wa kitaalamu wa kwamba tuanze kupembua njia ya kupitisha umeme tulipe fidia, tujenge majengo tuchukue na hatua nyengine; naomba Bunge lako Tukufu, liruhusu na kuielekeza Wizara iende ikakae na kuona kama muda huu unaweza ukaminywa kwa kuzingatia matakwa ya kitaalamu na bajeti tuliyojipangia ili wenzetu wa Katavi waweze kupata gridi hii kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, niongeze kwamba Mkoa wa Katavi unatumia umeme karibia Megawati 1 na kilowati kama 200, tutaenda kuona namna ambavyo tunaweza tukaongeza mashine na mitambo ya kuweza kufua umeme zaidi katika eneo hilo katika kipindi hiki ambacho bado tunaendelea na utengenezaji wa miundombinu yetu ya kufikisha gridi katika Mkoa wetu wa Katavi. (Makofi)
MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nami naomba kumwuliza Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati, Sengerema imekuwa inakatika umeme mara 30 kwa siku na tayari umeme umeshatengenezwa katika eneo letu la kupoozea umeme pale Pomvu Geita, kwa nini Sengerema msituunganishe katika laini ya Geita ili tukaacha kukatikiwa umeme kwa mfumo huu wa kukatika mara 10 kwa siku?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabasamu, Mbunge wa Sengerema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpe pole Mheshimiwa Mbunge kwa adha ambayo wananchi wake wamekuwa wakiipata, lakini kama nilivyosema tangu awali, Serikali imepambanua kwa muundo na msukumo mpya uliopo, haya matatio makubwa yataaenda kupunguzwa katika maeneo yetu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kukatika umeme kama nilivyosema, kunaweza kusababishwa na laini ya umeme kuwa ndefu au mazingira mengine kwa na vitu hatarishi kama maeneo ambayo ni oevu na tunafahamu maeneo mengi ya kanda ya ziwa ni oevu, kwa hiyo, nguzo zetu zimekuwa zikianguka au pengine laini kuwa na watumiaji wengi na pengine ikazidiwa. Kwa hiyo, mambo yote hayo yanachukuliwa maanani na kuangalia namna gani ambavyo tutaweza kurekebisha katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, namwomba Mheshimiwa Tabasamu aniruhusu baada ya hapa nikae nae niongee naye nichukue eneo lake kazi, ili nikakae na wataalamu tuweze kujua tatizo hasa linasababishwa na nini katika sababu mbalimbali. Maana inawezekana ukajenga kituo cha kupooza umeme katika eneo hilo, lakini bado umeme ukaendelea ukakatika kwa sababu tatizo halikuwa kituo cha umeme, pengine ilikuwa tatizo lingine, tukibaini tatizo lenyewe tutaweza kulifanyia kazi kwa usahihi.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwa kuzingatia taarifa iliyotolewa na Serikali ni kwamba kampuni iliyokuwa inafanya utafiti ya Beach Petroleum tangu mwaka 2017 imeshindwa kuendelea na kazi hiyo kutokana na kina kirefu cha maji na wenyewe kushindwa gharama hiyo: -

Je, Serikali imetafuta mwekezaji mwingine katika eneo hilo tokea hiyo 2017? Kama hivyo ndiyo, wananchi wategemee lini utafiti huo kukamilika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kilumbe Ng’enda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tangu mwaka 2017 pale ambapo kitalu kilirudishwa na mwenzetu wa beach petroleum mtakumbuka kwamba kulikuwa kuna upiatiaji wa mikataba ya uvunaji na ushirikiswaji (PSA) na hivyo tangu kipindi hicho Serikali haijatangaza vitalu wazi kwa ajili ya wawekezaji kuja kufanya utafiti katika maeneo hayo. Hivyo, baada ya PSA Review kuwa zimekamilika sasa Serikali iko tayari kuanza kutanganza ili watu sasa waweze kuja kuwekeza katika maeneo hayo kwa ajili ya kufanya utafiti na baadaye kubaini uwepo wa mafuta na kuanza kuyatumia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Kilumbe Ng’enga kwamba Serikali iko katika hatua za kuhakikisha inakamilisha hiyo taarifa ya PSA Review na baada ya kufanya reviews zikakamilika, itaweza kufungua kwa ajili ya kuweza kukaribisha sasa watu kuja kuendelea na utafiti. Itakapofanya hivyo, basi taarifa ya nini kimepataikana itatolewa. Nakushukuru.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Utafiti kama huo ambao umefanyika Ziwa Tanganyika umewahi kufanyika pia katika Ziwa Eyasi katika Jimbo la Karatu kuhusu upatikanaji wa mafuta katika ziwa hilo. Je, utafiti huo umekamilika au bado na je, matumaini ya kupata mafuta yapo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cecilia Paresso, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunalo bonde linaitwa Bonde la Eyasi Wembere ambalo linatoka Singida, linapita Tabora, linapita Simiyu na kipande cha Manyara pia kipo. Utafiti katika bonde hilo unafanywa na Shirika letu la TPDC na kwenye Bonde la Eyasi-Wembere bado tunaendelea na utafutaji wa awali wa kujua maeneo ambayo tunaweza tukapata mafuta au gesi katika maeneo hayo. kwa hiyo, utafutaji bado unaendelea na utakapokuwa umekamilika, basi utapata matunda ya kuweza kuvuna gesi na mafuta.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nakiri ni kweli nimeona kazi hiyo inaendelea katika kata hizo zilizotajwa. Pamoja na hayo nina maswali yangu mawili madogo ya nyongeza: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; katika utekelezaji wa miradi hii maeneo mengi ya huduma za jamii, hasa shule za msingi, shule za sekondari, makanisa na misikiti, hasa maeneo ambayo yako mbali kidogo na katikati ya miji, haziwekewi kipaumbele sana kupata umeme. Je, Serikali haioni kwamba ni vizuri kutenga bajeti maalum kwa ajili ya huduma za jamii, hasa sehemu ambazo watoto wetu wanasoma kwa sababu ni muhimu sana kuwa na umeme?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; katika miji mbalimbali midogo kwa mfano Mji wa Ilula uliopo Kata ya Nyalumbu, lakini pia Mji Mdogo wa Boma la Ng’ombe pamoja na Mji Mdogo wa Kidabaga, kumekuwa na kero kubwa ya kukatika umeme mara kwa mara. Je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza kero hii? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nyamoga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kwenye utekelezaji wa Mradi wa REA III, Mzunguko wa Pili, tuliwaelekeza wakandarasi wanaopeleka umeme katika maeneo yetu pamoja na wale wanaoshirikiana nao, wenzetu wa TANESCO, kuhakikisha kwamba maeneo ya taasisi na miundombinu mingine kama elimu, afya na taasisi za dini yanakuwa ni maeneo ya kipaumbele. Kama alivyosema Mheshimiwa Nyamoga, ni kweli maeneo yale ambayo tayari umeme umeanza kwenda kwenye maeneo ya makao makuu ya vijiji tayari tunapeleka.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Nyamoga pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine kwamba kadri tunavyozidi kupeleka umeme kwenye maeneo ya pembeni kwa maana ya vitongoji, tutazidi pia kufika katika taasisi hizo na ni maelekezo ya Serikali kwamba umeme ufike katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine la kufurahisha zaidi ni kwamba, sisi Wizara ya Nishati pia tumepewa kipande kidogo cha bajeti katika ile 1,300,000,000 za Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan zinazopeleka maeneo ya UVIKO tunaopambana nao na sisi katika miundombinu hiyo mipya ambayo inajengwa tumepatiwa pesa kiasi fulani ambapo tutaweza kuongeza kasi ya kupeleka umeme katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, ni kweli kwamba kumekuwa kuna makatizo ya umeme kwenye maeneo mbalimbali, lakini ni jambo ambalo lililopangwa kwa ajili ya kufanya marekebisho ya miundombinu. TANESCO katika mwaka huu wa fedha inazo bilioni karibu zaidi ya 200 kwa ajili ya marekebisho ya miundombinu ya umeme katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge waendelee kutuvumilia kidogo tukiwa katika hatua hizi na harakati za kuhakikisha tunaboresha miundombinu yetu. Na kwa Iringa tuna takribani bilioni moja na milioni 500 kwa ajili ya marekebisho ya miundombinu. Tutaendelea kuwahimiza wenzetu watoe taarifa sahihi na kwa wakati sahihi ili Waheshimiwa umeme unapokatika, basi wananchi waweze kufahamu nini kinaendelea. Nakushukuru.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Naomba niulize swali dogo tu la nyongeza. Kuna Mkandarasi anaitwa Giza mlituletea kwenye majimbo yetu, na mlimpa siku za kuja kwa Wabunge, mpaka leo tunamtafuta; nini kauli ya Serikali? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ni kweli nimepata concerns za baadhi ya Waheshimiwa Wabunge kuhusiana na Mkandarasi huyu Giza na kama alivyowahi kusema Mheshimiwa Mbunge mmojawapo kwamba jina la mkandarasi halivutii, lakini ni mmoja wa wakandarasi ambao walipata kazi katika Mradi wa REA II, round two katika Mikoa ya Manyara na Mara.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa wamekuwa wakiniuliza mara kwa mara. Nitoe taarifa kwamba, tumemtafuta na tumempa maelekezo mahususi, nikitoka hapa nitawaeleza Waheshimiwa Wabunge ni namna gani tumechukua hatua ili aweze kufanya kazi yake na kuimaliza, ili inapofika hiyo Desemba 2022 ambayo tumekubaliana naye, tusiwe nje ya muda huo.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii ili niulize swali dogo tu la nyongeza. Ni lini sasa mkandarasi ambaye majuzi tu

Mheshimiwa Naibu Waziri alituambia hapa katika Bunge lako Tukufu kwamba anaanza kazi katika Halmashauri za Wilaya za Manyoni na Itigi ataanza kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahaya kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuliwaelekeza wakandarasi wa lot hizo nne ambazo zilikuwa zimebakia, waripoti katika vituo vyao vya kazi wiki hii inayokwisha leo na ilikuwa ni kwenda kuangalia maeneo ya kupata go down za kutunza vifaa vyao na kuwasiliana na Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa Mbunge hajawasiliana na mkandarasi wake, naomba nitakapotoka hapa mimi mwenyewe nimuunganishe naye. Wiki inayokuja tunatarajia waanze kwenda kwenye maeneo hayo kwa ajili ya survey na kuanza kazi ambazo wameshasaini mikataba tayari. Nashukuru.
MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijauliza swali langu la nyongeza nimeshindwa kujizuia kumpongeza Dkt. Tulia Ackson kwa kuchaguliwa kwa kura zote kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, na Mwenyezi Mungu ambariki ili atekeleze haki za Watanzania hapa Bungeni. Baada ya hayo, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza, kwa majibu haya yaliyotolewa, mrai wetu huu wa kufua umeme wa Bwawa la Mwalimu Julius Nyerere hauwezi kukamilika kama mkataba ulivyosema. Tulipokuwa kwenye Kamati ya Bajeti mwezi wa 11 Waziri alikuja mbele ya Kamati akaieleza kwamba sababu za mradi huu kuchelewa ni Mkandarasi kukaidi dizaini iliyowekwa na wataalam ya kujenga mahandaki matatu kwa ajili ya kuchepusha maji, lakini badala yake alijenga handaki moja, jambo ambalo lilimfanya achelewe sana kukamilisha kazi hiyo, kwa hiyo ndiyo sababu kubwa ya msingi; na sababu za UVIKO-19 zilikataliwa; na majibu haya yako kwenye Hansard za Kamati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tena wamekuja na majibu mengine, wanasema kwamba ni kuchelewa kwa mitambo ya kubebea ile milango ya vyuma (hoist crane system), ndiyo iliyochelewa kufika na mradi huu kuchelewa kwa sababu ya UVIKO-19.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa sababu majibu haya yanakanganya, kwenye Kamati chini ya Hansard waliyakataa majibu hayo kwamba hayana ukweli wowote na wakasema kwamba majibu sahihi ni kwamba huyo alikuwa mzembe na kwamba watam-penalize kwa ucheleweshaji atakaoufanya wa kuchelewesha mradi huu ambao unacheleweshwa na Watanzania. Sasa Mheshimiwa Waziri atuambie; Kamati ni sehemu ya Bunge, na hapa wamekuja na majibu mengine, na ushahidi wa Hansard upo. Nini majibu ya Serikali ya kuchelewesha mradi huu, kwa sababu majibu mawili tayari yametolewa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, ni kuhusu katakata ya umeme inayoendelea na mgao wa umeme unaoendelea hivi sasa. Mwanzo tulielezwa kwamba sababu ya mgao wa umeme unaoendelea sasa hivi ni kwa sababu ya matengenezo ambayo hayakufanyika kwa miaka mitano, ndiyo maana wako kwenye maintenance. Baada ya muda mfupi tena tukaambiwa kwamba ni kwa sababu ya mabwawa yanayotumika kufua umeme kukauka na yamekauka kwa sababu ya mifugo pamoja na ukaidi wa binadamu. Sasa hivi tena, wakati huo huo TANESCO nao wanasema kwamba hakuna mgao wa umeme, baadaye TANESCO wanatangaza mgao wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hebu tuelezwe na Serikali; kwa sababu suala la katakata ya umeme na mgao wa umeme hivi sasa linaathiri sana Watanzania; viwanda vinafungwa, wananchi wako kwenye dhiki kubwa, huduma za afya zimevurugika, huduma za maji zimevurugika. Kwa ujumla Taifa liko kwenye hali ngumu ya ukosefu wa umeme…

MWENYEKITI: Umeeleweka Mheshimiwa, umeeleweka.

MHE. LUHAGA J. MPINA: …tupate majibu sahihi ya Serikali ni nini kinachosababisha hali hii ya kukatikakatika kwa umeme kuendelea?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianze na swali la kwanza, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, mradi kwa mujibu wa mkataba unatarajiwa kukamilika tarehe 14 Juni, 2022. Wazungu wanasema do not cross the river before you reach there. Muda utakapofika kama mradi hautakamilika hatua za kisheria za kimkataba zitachukuliwa kwa aliyesababisha ucheleweshaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, lilikuwa linajitegemea, liliulizwa kwa nini maji hayakujazwa kufikia mwezi Novemba na sababu za kueleza kwamba cranes na milango vilichelewa kwa sababu ya UVIKO ni sababu pekee ya kuchelewesha kuziba diversion channel iliyokuwa inachepusha maji. Kwa hiyo maelezo hayo hayahusiani na mradi mzima, kwamba mradi umechelewa. Kama nilivyosema, muda wa kukamilisha mradi bado haujafika na tutakapofikia mto tutaivuka kutokana na mazingira yatakayokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu kwamba hakuna taarifa zinazokinzana, isipokuwa taarifa zote hizi kwa pamoja zitashughulikiwa kulingana na muda utakavyokuwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu swali la pili, kuhusu kukatika kwa umeme; kwanza niombe kutoa maelezo ya Serikali, kwamba TANESCO haikatikati umeme, hakuna mtu ambaye ameajiriwa kwa ajili ya kukata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mifumo ya umeme ina-respond kulingana na mazingira. Kikubwa zaidi kinachotokea ni kwamba pale ambapo mitambo yetu inazidiwa na matumizi yenyewe automatically inakata umeme. Sasa tunapokwenda kuangalia tatizo ni nini, tukilibaini basi tunawasha. Miongoni mwa tatizo ambalo limekuwa likitokea ni kwamba, mara nyingi mitambo inapokuwa imepata mzigo mkubwa ikakata umeme na wale watumiaji nao wenyewe wanazima vifaa vyao.

Kwa hiyo sisi tukirudi kwenye mtambo wetu tukawasha unakubali kuwaka kwa sababu mitambo inakuwa haipo. Sasa wale wenzetu wakiwasha tena inakata tena. Kwa hiyo pengine inaonekana kama kuna mtu anakata na kuwasha, lakini ni system yenyewe ina-respond. Tunachokifanya ni kuhakikisha kwamba tunaongeza nguvu zetu za mitambo ili kuweza ku-capture sasa mahitaji tuliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie kidogo suala la kwamba tulisema maji, sasa tukasema gesi. Ni kwamba tulitarajia kuwa kwenye marekebisho ya mtambo yetu ya kufua gesi ambayo inazalisha sehemu kubwa sana ya umeme hapa nchini tuiongeze kwa sababu sasa tuna uwezo wa kuongeza megawatt takriban 290, twende tukarekebishe kwenye visima vyetu vya gesi ili sasa tuweze kupata gesi nyingi zaidi kwa sababu ya kutokuwa na hali nzuri ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme. Ule mgao au matarajio makubwa ya mgao tuliodhani tutakuwa nao hatutakuwa nao; na sababu kubwa za kutokuwa na mgao huo ni tatu. Jambo la kwanza, tumekaa pamoja na wataalam, kwa maelekezo ya Mheshimiwa Rais kwamba mgao usiwe mkali kiasi kile, tukabaini kwamba tunaweza tukapata ile gesi iliyokuwa kwa wenzetu wa PAET ambao ndio watakaokwenda kurekebisha mitambo yao, tukapitisha baadhi ya kiwango kidogo cha gesi kupitia mitambo yetu ya TPDC na hivyo kufidia upungufu wa gesi ambao tungeupata. Hiyo imekuwa ni sababu ya kwanza, kwamba lile pengo kubwa ambalo tungelipata kwa kutokuwa na gesi tutalipunguza kupitia gesi na kuichepusha kwa kupitia njia ya TPDC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tunaliona, sisi sote ni mashahidi kwa sasa, hali yetu ya mabwawa imeanza kurudi katika hali nzuri na hivyo itaweza kutusaidia kujazia sasa kwenye maeneo ambayo yanatakiwa yapate umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu, umeme ni supply and demand. Tulitarajia kwamba kutakuwa kuna mahitaji makubwa sana ya umeme. Kuna kitu kinaitwa load flow analysis. Yulipoifanya load flow analysis tulibaini kwamba kile tulichokitaratjia kitahitajika sicho ambacho kitahitajika. Baada ya kuwa tunahitaji takriban 280 hadi 300 tunaona zitakazohitajika ni kama megawatt 100, ambazo katika mfumo wa kawaida huwa hazipo hapa na pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nitoe kauli ya Serikali, ule mgao ambao tuliutarajia utakuwepo kwa makali yale na ukubwa ule hautakuwepo na tutahakikisha kwamba watu wanaendelea kupata umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niseme, katika kipindi hiki ambako kutakuwa na mgao mdogo au kutokuwepo kwa umeme katika maeneo mbalimbali tutaitumia vizuri nafasi hiyo ili kufanya mambo kadhaa yanayoboresha mfumo wetu. Mojawapo ni kuhakikisha tunapunguza mzigo katika njia za umeme tunazoziita feeder, zile ambazo zimezidiwa kutoa sehemu moja kwenda sehemu nyingine, kukatia miti na mapori ambayo yamekuwa yakiangukia maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuboresha vituo vyetu vya kupoza umeme. Kama jana tulifanya cha Muhimbili, leo tunafanya pale Kunduchi na kesho kutwa watafanya pale Ubungo ili kuhakikisha kwamba tutakaporudi katika hali ya kawaida baada ya wiki moja ama mbili, tunarudi katika hali nzuri ambayo itakuwa bora kwa watu wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali hili niliuliza kwa sababu kuna kata nyingi sana kule ambazo hazijapata umeme hususani Kata ya Uwilo kuna vijiji kama viwili vile Lukulu Skimosoni na kule Maruhango pia kuna vijiji maruhango kwenye hakuna umeme je, niulize ni lini hasa vijiji hivyo vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Pallangyo na nimshukuru kwa ufuatiliaji na uvumilivu kwa sababu jimbo lake ni moja ya majimbo ambayo mkandarasi alichelewa kupatikana kwa sababu ya taratibu ya kimanunuzi. Lakini kama nilivyosema kwenye swali na jibu la msingi ni kwamba kufikia Disemba mwaka huu kwa mujibu wa mkataba kata zote ambazo hazina umeme ambazo ni vijiji kwakwe ni vijiji 12 ndiyo havina umeme vitakuwa vimepatiwa umeme kwa kadri ya mkataba tuliokuwanao.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilini Serikali itajenga substation ya kule Mkuranga sambamba na kuweka transformer ya NVA 90 pale katika substation ya Mbagala ili kuondoa tatizo la ukatikaji wa umeme mara kwa mara katika jimbo la Mbagala?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, jimbo la Mbagala linalo substation ndogo kama alivyosema ambayo ina transformer yenye uwezo wa AVA 50 NA substation hiyo inapeleka umeme mpaka maeneo ya mkulanga na kwa bahati nzuri ambayo inakuwa mbaya kwa upande mwingine. Eneo la Mkulanga limekuwa na viwanda vingi sana na hivyo linachukua umeme mwingi sana kutoka eneo la Mbagala.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshaanza upembuzi wa kujenga kituo cha kupoza umeme eneo la Mkulanga ambacho kitakuwa kina zaidi ya Megawatt 100 lakini taratibu za kukamilisha ununuzi wa transformer ya AVA 90 itakayokuja kufungwa pale Mbagala zinakamilika na tunaamini kabla yam waka huu kuisha kituo cha Mbagala kitakuwa kimeongezewa uwezo wakati kule Mkulanga substation ikiwa inapatikana fedha kwa ajili ya kuanza kwa ujenzi.
MHE. MICHAEL J. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na sinto fahamu kubwa juu ya kiwango gani kitozwe kwa wananchi ili kuweza kuvutiwa umeme kwenye maeneo mbalimbali wakiwemo wananchi wa eneo la Nasio Wilaya Ukerewe. Nilitakakujua ni vigezo gani vinavyotumika kujua ni kiwango gani cha pesa kinatakiwa kulipwa na mwananchi ili aweze kuvutiwa umeme kwenye eneo lake la nyumba.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mkundi kwa swali lake nzuri Mbunge wa Ukerewe ambaye pia amekuwa akifuatilia sana mambo ya umeme katika jimbo lake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka tulikuwa tume standardize gharama za upatikanaji wa umeme lakini baadaye tulimuomba Mheshimiwa Rais atukubalie tufanye marekebisho katika baadhi ya maeneo ili kuweza kufanya kazi hii kwa ufanisi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumerudi kwenye vile viwango ambavyo tulikuwa tunavitumia hapo awali ambapo maeneo ya mijini yanapata umeme kwa gharama ambazo wenzetu wa EWURA ndiyo wa simamizi wa gharama wameziweka zinaanzia laki tatu na kuendelea. Lakini maeneo ya vijijini yanapata umeme kwa gharama ya shilingi elfu saba kwa line ya njia moja na gharama nyingine zile za kawaida kwa njia tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwango na vigezo ambavyo tunavitumia viko katika sheria ya mipango miji ile ndiyo inayosema hapa ni jiji hapa ni mji hapa ni Kijiji na hapa ni nini. Kwa hiyo, kwa kutumia sheria hiyo ambayo inatumiwa na wenzetu wa TAMISEMI na watu wa ardhi tunaitumia hiyo sasa ku-decide kwamba hapa itakuwa 27 hapa itakuwa zile gharama za mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajipanga kuendelea kutoa elimu kubwa Zaidi ili wananchi waweze kuelewa kwamba kiwango gani kinatozwa wapi na kwa sababu zipi kwa mfumo huo niliousema kwa hapo.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, amekuja kuzindua umeme katika Jimbo la Mbulu Vijijini. Lakini nataka nimtaarifu kwamba pamoja na kuja kuzindua ule umeme baada ya kuondoka hakuna kilichoendelea, maana yake mkandarasi hayuko site.

Je, atafanya nini ili walau mkandarasi yule arudi site aweze kuendelea kuunganisha vile vijiji ambavyo mkandarasi amesaini kama mkataba?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ziko kata ambazo kwa kweli zina hali mbaya na uliahidi kwamba umeme utafika; ni lini hasa zile kata ambazo wewe mwenyewe alitamka wakati anazindua umeme Mbulu Vijijini zitapata umeme? Maana sasa hivi kama nilivyosema, wakandarasi hawako site. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nimpongeze Mheshimiwa Massay kwa sababu kweli tulikwenda kuzindua umeme katika jimbo lake na tulizindua umeme katika Kijiji kinachoitwa Munguhai, ni eneo zuri sana, na uwepo wa Mungu ulionekana kweli katika kijiji hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwamba mkandarasi anapopewa kazi ya REA kuna awamu kama nne za kufanya. Baada ya kusaini mkataba mkandarasi anakwenda site kufanya survey ili kubaini kama ile kazi iliyoandikwa kwenye karatasi ndiyo hasa ile ya kufanyika kazini. Na hiyo mara nyingi inachukua miezi mitatu mpaka mitano kulingana na hali ya hewa, eneo linavyofanana na wigo wa upana wa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo linafanyika baada ya hapo, wanakwenda kufanya uhakiki watu wa TANESCO, REA pamoja na mkandarasi mwenyewe, wanashirikiana kuona kama kilichoonekana site ndicho hicho hasa ambacho kinatakiwa kifanyike na wanakubaliana. Baada ya hatua hiyo, inakwenda sasa kwenye ununuzi wa vifaa. Baada ya vifaa kupatikana ndiyo sasa tunakwenda kwenye utekelezaji wenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi hatua tatu nilizozitaja za kwanza za survey, kwenda kwenye kufanya uhakiki na ununuzi wa vifaa unachukua miezi nane mpaka kumi kukamilika. Niwaombe Waheshimiwa Wabunge, najua kwenye maeneo mengi hatua hizi ndiyo sasa zinaelekea kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengi sana ambapo wakandarasi watakuwa hawaonekani site, siyo kwamba wame-abandon site, hapana, watakuwa kwenye moja wapo ya hizo hatua ambapo pengine hawaonekani kuwepo sana katika maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niwahakikishie kwa maelekezo yaliyokuwepo mikataba yote inatakiwa ikamilike Desemba mwaka huu na tunatarajia kuanzia mwezi Machi mwanzoni wakandarasi wengi watakuwa wamemaliza zile hatua za manunuzi na survey na watakuwa wamefikisha vifaa site wataanza kuonekana wakifanya kazi kwa miezi nane mfululizo ili kazi hizo ziweze kukamilika kwa wakati. Kwa hiyo na ndugu yangu, Mheshimiwa Mbunge wa Mbulu Vijijini atakuwa kwenye category hiyohiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kwenye eneo la pili kama nilivyosema tangu mwanzo, vijiji vyote ambavyo havina umeme vitapatiwa umeme kabla ya Desemba na vijiji vingine vilivyopo kwenye kata alizozitaja vikiwemo. Nashukuru.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kuna mkanganyiko mkubwa kuhusu bei ya umeme vijijini; kwa nini Serikali isitoe tamko hapa Bungeni ili wananchi wote wanaoishi vijijini waelewe bei ya umeme vijijini ni shingapi, ni shilingi 27,000 au ni hiyo 300,000? Ili kuondokana na sintofahamu inayowapata wananchi wa vijijiji.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa Mwenisongole kwa swali lake zuri na kwa ufuatiliaji wa mambo yanayowahusu wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeshatoa tamko na mimi nilirudie; umeme vijijini ni shilingi 27,000 kwa njia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena; kwa single phase vijijini umeme ni shilingi 27,000. Ilikuwa jana na itakuwa leo na kwa hali ilivyo sasa na maelekezo tuliyonayo itakuwa hivyo kesho, shilingi 27,000. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa nafasi hii nami niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Serikali itupe ufafanuzi kidogo; pamoja na ufafanuzi uliotolewa wa shilingi 27,000 katika vijiji lakini kabla ya hapo kulikuwa na bei tatu; kulikuwa na 320,000; 177,000 kwenye vimiji vidogo kama Itigi na 27,000 kwa vijiji. Sasa wametoa wale wa 177,000 wamewapeleka kwa 320,000; vijiji ambavyo vimeungana vijiji vitatu vinne kwa kuwa tu vina kasoko basi vinaonekana ni mji vilipe 320,000/-. Je, Serikali iko tayari sasa kukubaliana na bei zilizokuwa kabla ya kurudi 27,000 na kuwa 177,000 kwa miji midogo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa swali zuri kutoka kwa Mheshimiwa Massare. Ni kweli hata kabla ya hapa tayari sisi kama Wizara kwa niaba ya Serikali tumeshapata mapendekezo na maoni na maombi mbalimbali ya ku-vary hizi gharama ambazo tuko nazo sasa. Na wengine wakaenda kwenye kupendekeza kwamba hata mtumishi wa Umma anavyolipwa posho anapoenda kwenye jiji, manispaa au wilaya, zile posho anazopewa zinatofautiana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Serikali niseme tumelipokea na tutakwenda kulifanyia kazi ili kuangalia uhalisia wa maisha tunayoishi sasa na gharama ambazo Serikali inaweza ikazitoza ili wananchi waweze kupata huduma hii ya umeme kwa gharama nafuu ambayo inamfikia kila mtu. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi ambapo REA wamepeleka umeme wamepitisha laini kuu na pale chini kwa wananchi wa kawaida hakuna umeme. Kwa mfano nimueleze Mheshimiwa Waziri, nina vitongoji 610, vitongoji ambavyo havijafikiwa ni 503 na ukija kuangalia wanasema vijiji karibu asilimia zaidi ya 75 vimeshapata umeme, lakini ukiangalia wananchi wengi hawana umeme na mahitaji ni makubwa. Ni lini hivi vitongoji vitapelekewa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, na ninamshukuru kaka yangu, Mheshimiwa Bilakwate, kwa swali zuri kabisa, na mimi Kyerwa ninapafahamu. Lakini ninaomba Mheshimiwa Bilakwate achukue tu na kuamini maelezo aliyoyatoa Mheshimiwa Waziri, kwamba tunafahamu kwamba vitongoji vingi sana havina umeme na plan na mkakati mkubwa sana wa Serikali wa kufikisha umeme katika vitongoji hivyo vyote ndani ya miaka minne upo na unaendelea na utakapokuwa tayari vitongoji vyote 37,000 nchini ambavyo havina umeme vitapatiwa umeme.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na nina maswali mawili madogo ya nyongeza. Kwanza niishukuru Wizara ya Nishati hasa Mheshimiwa Rais, Makete tulikuwa na vijiji 37 havina umeme, lakini mkandarasi amekuja na anaendelea kazi vizuri, lakini changamoto ambayo tuko nayo, swali la kwanza, ni kwa mkandarasi wa REA phase III round one ambaye hadi sasa hajakamilisha kazi ya kusambaza umeme kwenye vijiji baadhi ya Makete. Je, ipi kauli ya Serikali kwa mkandarasi huyo ambaye hadi dakika hii amefelisha zoezi la kusambaza umeme kwenye vijiji kadhaa?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Makete tulipewa bwawa la umeme la Lumakalia sisi tunaita bwawa la Luvaninya, hili bwawa kwa muda mrefu limekuwa likitamkwa wananchi wangu hawajajua hadi sasa hivi ni lini linaanza kujengwa. Sasa naomba kauli ya Serikali, ni lini Serikali itaanza kujenga bwawa hili ambalo linaenda kutatua kero ya umeme kule Makete na mikoa ya karibu kama Mbeya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Festo Sanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza, nipende kupokea shukrani alizozitoa kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan za kuhakikisha kwamba umeme unafika katika vijiji vyote na sisi kama Serikali tunaendelea kumsaidia Mheshimiwa Rais kutekeleza majukumu ambayo ametupatia.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba REA III round ya kwanza kuna maeneo hayajakamilika. Zilikuwepo lots 29 na zilizokamilika kabisa ni lots 21, lots nane bado hazijakamilika na eneo la Makete likiwemo. Kauli ya Serikali ni kwamba tumeingia mkataba wa nyongeza ya muda kidogo na wakandarasi na tumekubaliana nao ifikapo Machi mwaka huu, kazi zote zimekamilika.

Mheshimiwa Spika, niseme moja wapo ya sababu kubwa ambayo ilichelewesha miradi hii ni UVIKO ambao ulichelewesha vifaa kupatikana, lakini sababu nyingine kubwa ambayo ilikuwa inatokea ambayo maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan tumeyatekeleza na kubadilisha utaratibu REA III round one ilikuwa inaenda kwa utaratibu unaoitwa goods na siyo works, yaani wakandarasi walikuwa wanapewa pesa, wanunua vifaa ,wakishafikisha vifaa ndiyo sasa tunaanza kuwapa utekelezaji wa kazi. Hii imepelekea sasa wakandarasi wengine washindwe kufanya kazi na mikataba yao ikabidi tuivunje ili kupata wengine, kwa hiyo muda ukapotea.

Mheshimiwa Spika, kwenye REA III round II maelekezo tuliyoyapata na tutayatekeleza ni kwamba, mradi unatekelezwa kwenye utaratibu wa works, mkandarasi analipwa kwa kile kiwango cha kazi aliyofanya na tunaamini hiyo itatusaidia kukamilisha kazi zetu zote tulizonazo kwa wakati kwa sababu usipokamilisha kazi inabakia kazi sawa na pesa ambayo haujaifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, ni kweli kwamba kule Makete na maeneo mengine ya Njombe kuna Mradi unaitwa Rumakali ambao Serikali inatarajia kuutekeleza na pale tutapata Megawatts 222. Feasibility ya pale ilifanyika mwaka 1998 na kwa kuwa tumeona uwezo wa kupata fedha wenzetu wa TANESCO wamemweka Consultant mpya wa kufanya update ya ile feasibility study ili tuendane na hali ya sasa. Kwa hiyo, kinachofanyika sasa, mkandarasi wa feasibility study ameanza kazi yake Januari, tunatarajia atamaliza mwezi wa Tano na kuanzia mwezi wa Tano itaanza kufanyika evaluation kwa ajili ya compensate wale watu walioko maeneo yale.

Mheshimiwa Spika, tunatarajia mwishoni mwa mwaka huu mambo yote yatakuwa yamekamilika, hivyo mwaka ujao pesa ya kujenga mradi itakuwa imepatikana na tunaweza kuanza kutekeleza mradi huo kwa ajili ya kuongeza umeme unaozalishwa kwenye maji katika Gridi ya Taifa.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona. Napenda kuuliza na kujua tatizo lililopo hasa TANESCO kwa upande wa Morogoro Mjini; baadhi ya wananchi wamelipia umeme kuwekewa kwenye nyumba zao lakini imechukua muda mrefu hawajawekewa mpaka sasa hivi. Kwa mfano, Kata ya Kasanga kuna wananchi wamelipia lakini mpaka hivi sasa hawajawekewa: -

Je, kuna tatizo gani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Christine Ishengoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba wapo wateja ambao wamelipia huduma ya TANESCO lakini walikuwa hawajaipata na hii ni kutokana na kwamba kulikuwa kuna mwamko mkubwa sana kwa wananchi wanaohitaji umeme na uwezo wetu TANESCO kidogo ulikuwa umepungua kwa sababu ya kutokuwepo na vifaa vya kutosha kukamilisha kazi hizi.

Mheshimiwa Spika, tayari Mheshimiwa Rais ameshaelekeza, Wizara yetu inasimamia TANESCO kuhakikisha kwamba vile viporo ambavyo ni vya nyuma angalau visiwepo zaidi ya miezi mitatu iliyopita. Yaani mtu akilipa Februari hii, angalau mwezi Machi au Aprili awe ameunganishiwa umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Dkt. Ishengoma pamoja na Wabunge wengine wote kwamba Serikali inajitahidi kuhakikisha kwamba vile viporo vya kuunganisha umeme vinaunganishwa na kukamilika ndani ya muda mfupi ili kila mtu aweze kunufaika na umeme ambao unazalishwa.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na jitihada kubwa ambayo imefanywa na Mheshimiwa Rais kupitia Wizara ya Nishati kusambaza umeme kwa kiwango kikubwa, lakini changamoto kubwa ni kwamba inaonekana fedha hazitoshi kwa ajili ya usambazaji wa umeme kwa line ndogo ndogo.

Mheshimiwa Spika, Wizara ina mkakati gani wa kuhakikisha kwamba inapata fedha ili wananchi hawa sasa wafaidi umeme kupitia line ambazo zimeshajengwa nchini Tanzania?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Engineer Manyanya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba mahitaji ni makubwa lakini pesa haitoshi. Hata hivyo, Serikali ya Awamu ya Sita tayari imetoa shilingi 1,250,000,000,000 kwa ajili ya upelekaji wa umeme katika vijiji. Hivyo, tunaamini pesa angalau ipo ya kutosheleza mahitaji kadhaa tuliyokuwa nayo.

Mheshimiwa Spika, kama alivyosema juzi Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kwamba sisi Wizara ya Nishati tunao mkakati mkubwa ambao baadaye utakuja kuwasilishwa kwa Mheshimiwa Rais na kwenu, kwamba tunatafuta fedha kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji vyote nchini na makadirio yetu yanaonesha ni kama shilingi trilioni saba na nusu. Tunaamini kwa sababu tunakopesheka, tunaaminika kwa Mataifa mengine na tunahitaji kupeleka umeme kwa wananchi wetu, fedha hiyo tutaitafuta na tutaipata kwa ajili ya kuhakikisha kwamba kila mwananchi anayehitaji umeme anaupata.

Mheshimwia Spika, Mheshimiwa Waziri alisema, angalau ifikapo 2025 jambo hilo liwe limekamilika, Mheshimiwa Rais akisimama basi kura zimwagike kwa ajili ya kushinda vizuri.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniona. Utekelezaji wa REA III, round ya pili Jimbo la Mbinga unakwenda kwa kusuasua sana. Mpaka nakuja hapa Mkandarasi alikuwa bado hajafanya chochote.

Nini kauli ya Serikali juu ya Mkandarasi huyu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kapinga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wakandarasi wa REA wanazo hatua kadhaa za utekelezaji wa miradi. Wanafanya survey, wanafanya uhakiki, wananunua vifaa na baadaye wanaanza kujenga. Hizi hatua tatu za mwanzo mara nyingi hawaonekani site, wanapoanza kujenga ndiyo wanaonekana. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba Mkandarasi atakuwa kwenye mojawapo ya hatua hizo na kabla ya mwezi Machi ataonekana site kwa ajili ya kuendelea na kazi ambayo tayari amepewa kwa sababu deadline yake ni mwezi wa Desemba, 2022 na tunaamini ataikamilisha.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa kuwa katika Wilaya ya Mbarali kuna uzalishaji mkubwa wa mpunga na viwanda vingi vya kuchakata mazao ya mpunga, lakini umeme ni hafifu kwa maana ni low voltage.

Je, Serikali iko tayari kufunga transformer kubwa ili kusudi kuwasaidia wananchi wa Mbarali ambao wana bidii katika kuzalisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kutokana na kwamba Serikali hivi karibuni ilitangaza bei mpya na bei hii ni kwa ajili ya maeneo ya mijini na maeneo ya vijijini bado bei itabaki ile ile ya shilingi 27,000/= kwa umeme unaosambazwa na Wakala wa Umeme Vijijini; hata hivyo, sheria inayotumika kuamua kwamba hili ni eneo la mji, kwa maana ya Sheria ya Urban Planning Act. No. 8 ya Mwaka 2007, inasema kwamba eneo litahesabika kuwa ni mji ikiwa lina maduka kuanzia 20 na kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo kama Mafinga Mjini, ambapo maeneo kama Vijiji Ndolezi, Makalala, katika Sheria hii ya Serikali za Mitaa inahesabika kwamba hilo ni eneo la mji, lakini maisha halisi ya wananchi ni ya kijijini. Kwa mfano, hapa Dodoma kuna Kata 41; Kata za mjini ni 15 tu, the rest maisha yao ni ya kijijini kabisa: Je, Serikali ina mpango gani kuangalia maisha halisi ya wananchi ambao pamoja na kuwa inasemekana wapo mjini kutokana sheria hii, lakini maisha yao ni ya kijijini ili nao waweze kulipa shilingi 27,000? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Cosato Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza, ni kweli tunalo tatizo la voltage katika maeneo mengi hapa nchini na tayari Serikali imechukua jitihada za makusudi kabisa za kufanya kitu kinachoitwa voltage improvement kwa kuongeza vituo vya kupooza umeme na kufunga mitambo inayoitwa Auto Voltage Regulators kwenye maeneo mbalimbali ili kuweza kufikisha umeme mwingi zaidi kwa wanaohitaji. Kwa hiyo, eneo la Mbarali ni mojawapo ambalo lipo katika mpango huo na hiyo kazi itafanyika. Namwomba Mheshimiwa Mbunge aendelee kuvumilia kidogo na huduma nzuri itafika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, kama alivyosema yeye mwenyewe, sheria inaeleza kama alivyosema; na sheria tulitunga sisi wenyewe hapa Bungeni; lakini uhalisia ni vyema ukaangaliwa na sisi kama tulivyosema siku zilizopita, jambo hili tumelichukua na tumewakabidhi wenzetu wa TANESCO waangalie upya uhalisia unavyosema ili pamoja na sheria kuwepo, tuone namna ambavyo sheria hii itawatumikia wananchi ambapo ndiyo hasa tuliitengeza ili iwalinde wao na kuwahakikishia huduma nzuri. Nashukuru. (Makofi)
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa hii nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Kwanza nianze kwa kuishukuru Serikali kwa kuweka bayana bei ya umeme vijijini ni shilingi 27,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni hili; hapa katikati kuomeongezwa bei ya umeme mijini kutoka shilingi 177,000 mpaka shilingi 320,000.

Je, Serikali haini kama hiyo bei kwa watu wanaoishi mijiji nao bado ni kubwa sana? Kwa nini isirudi bei ya awali ya shilingi 177,000 ili wananchi wa mijini nao kwa wingi wapate nafasi ya kuunganishiwa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwanisongole kama ifutavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, majibu niliyoyatoa kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, kimsingi ndiyo yanayokwenda mpaka kwenye swali la Mheshimiwa Mwenisongole. Tunakwenda kuangalia kwa ujumla maeneo ni yapi na gharama ipi iweze kutumika katika maeneo hayo ili kuwahakikishia wananchi wote huduma hiyo kwa gharama nafuu ambayo wataiweza. (Makofi)
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa niaba ya wananchi wa Wilaya ya Temeke, hasa Jimbo la Temeke, naomba kuuliza: Je, ni lini sasa umeme utakamilika kwenye Jimbo letu la Temeke? Kwani hata kabla ya mgawo tulikuwa hatupati umeme; na sasa pia hatupati umeme kwa masaa mengi zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Temeke wanataka kujua; je, ni lini sasa kutakuwa na ukamilifu wa umeme kwenye Jimbo letu la Temeke? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dorothy Kilave, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kumekuwa kuna outage kadhaa ndani ya Jimbo la Temeke. Sababu ya kukatika kwa umeme mojawapo ilikuwa inasababishwa na ujenzi wa barabara ya BRT ambapo tumekuwa tuna schedule ya kukata umeme katika siku ya Jumanne na Alhamisi kwa ajili ya kupisha uhamishaji wa nguzo kwa ajili ya utengenezaji wa barabara hii. Pia zoezi hilo limekuwa likiendana pamoja na kuhamisha ile miundombinu ya umeme kuipitisha chini ya ile barabara na kuweza kuweka mazingira mazuri ambayo yatakuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hilo linakwenda sambamba na uboreshaji wa miundombinu ya umeme katika Jimbo la Temeke na mkoa mzima wa Dar es Salaam kwa kujenga vituo vya kupoozea umeme na kuviongeza nguvu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika muda mfupi ujao kama nilivyojibu juzi, kwamba tutakuwa tumeweka vizuri mazingira ya umeme kwenye Mkoa wetu wa Dar es Salaam na katika maeneo mengine kwa kurekebisha miundombinu mbalimbali. (Makofi)
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali mawili ya nyongeza. Kasi ya kusambaza umeme kuwafikia wananchi imekuwa ikisuasua kinyume na ahadi tuliyokuwa tukiambiwa kwamba tutawafikia wananchi wote kwa wakati mmoja; na yote hii inasemekana ni ukosefu wa fedha: Je, ni lini Serikali itawapelekea umeme wananchi wa Jimbo la Kalenga Mkoani Iringa hasa vitongoji vya Irangi, Unyangwila, Wambi, Ilongimembe na Igawa pamoja na Kata za Magulirwa na Kihanga? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wakazi wote wanapata umeme? Tumeona kwamba wakileta umeme katika Kijiji wanatoa kwa nyumba tatu au nne halafu wanaruka, wanakwenda sehemu nyingine, wanaruka. Sasa ni mkakati upi wa Serikali wa kuhakikisha kwamba nyumba zote ambazo zinahitaji umeme zinapata? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tendega kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kusema kwa niaba ya Serikali kwamba miradi yetu ya REA na upelekaji wa umeme vijijini haisuisui; na hizo rumors kwamba hakuna fedha, siyo za kweli. Katika awamu ya tatu mzunguko wa kwanza, miradi 28; jumla ya Lot 28 zilitekelezwa na asilimia kubwa zimekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipindi hiki ambacho tupo, jumla ya Lot 39 tayari mikataba yake imesainiwa na takribani shilingi trilioni 1,250 zipo tayari kwenye mikataba na Wakandarasi wanaendelea na kazi katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo, suala la uhaba wa fedha halipo. Fedha ipo na umeme utafikishwa katika maeneo yote kwa kadri ya muda ulivyopangwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la pili, ni kweli kwamba siyo kila anayehitaji umeme ameupata kwa sasa, lakini kama ambavyo tumekuwa tukisema hapa, Serikali ya Awamu ya Sita itajitahidi sana kuhakikisha kwamba fedha inapatikana; na mbinu nyingine za ubunifu zimekuwa zikitumika kuishauri Serikali. Tulisema juzi kwamba tunatarajia kufika 2025 kwa kadri tulivyojipanga, Serikali itakuwa imefikisha umeme katika vitongoji vyote kwa kutumia takriba shilingi trilioni 7,500 kama tulivyosema kwamba tutakwenda kutafuta sehemu ya kupata hizo fedha kwa ajili ya kupeleka umeme huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimalizie kwa kumshukuru Mheshimiwa Kiswaga kwa sababu maeneo yote ambayo yamesemwa amekuwa akiyafuatilia pamoja na Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali hilo kwa niaba ya wananchi wa Kalenga. Nashukuru. (Makofi)
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Japokuwa Serikali imekuwa ikiweka jitihada kubwa kwa kuhakikisha kwamba vijiji vya Mkoa wa Kagera vinapata umeme kupitia REA, lakini ukweli ni kwamba hata kabla ya mgao huu Mkoa wetu wa Kagera umekuwa ukikaa gizani siku mbili, tatu mpaka nne kila wiki na hii inatokana na kwamba bado Mkoa wa Kagera haujaungwanishwa kwenye Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi cha mwaka 2021 hapa Bungeni niliuliza suala hili na Serikali waliahidi kwamba mwaka 2022 Mkoa wa Kagera utaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa. Kwa hiyo, napenda kupata kauli ya Serikali: Je, ni lini Mkoa wa Kagera utaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa ili tuondokane na adha ya kuwa gizani? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza swali la Mheshimiwa Neema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera unazo Wilaya saba na Wilaya mbili tu za Biharamuro na Ngara ndiyo zinapata umeme wa gridi. Wilaya tano zilizobaki zinapata umeme kutoka Gridi ya Taifa la Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jitihada kubwa sana ambazo zinafanywa na Serikali ni kuhakikisha kwamba Mkoa wa Kagera unaunganishwa na Gridi ya Taifa kwa kutoa umeme katika eneo linaitwa Benako kwa kuchota kwenye line inayotoka katika mradi wetu wa Rusumo kwenda Nyakanazi. Tayari eneo la kupitisha kilometa 179 za line kubwa ya Kilovolt 220 zimeshatengenezwa, survey imeshafanyika na umeme ule utaletwa katika kituo chetu cha kupooza umeme cha Kyaka na Mkoa wa Kagera katika muda mfupi wa miaka miwili utakuwa umeunganishwa katika Gridi ya Taifa. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa nafasi. Naomba nimwulize Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Serikali ina dhamira njema sana ya kupeleka umeme vijijini na kwa kuwa Mkandarasi wa Wilaya ya Manyoni ambapo kuna majimbo mawili; Manyoni Mashariki na Manyoni Magharibi ambapo mimi nipo, Mkandarasi wake alichelewa kuanza kazi na toka ameripoti hatuoni kitu kinachoendelea: Je, Serikali iko tayari kumhimiza aanze kazi haraka?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Massare kama ifuatavo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inawahimiza sana Wakandarasi wote kukamilisha kazi zao kwa wakati kwa mujibu wa mkataba na tunaamini hakuna atakayechelewa na atakayechelewa hatua madhubuti zitachukuliwa kwa mujibu wa mkataba.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuniona. Majimbo mengi yaliyopo mjini, mengine yana kata ambazo zipo vijijini na kuonesha kwamba kata hizo zipo kwenye maeneo ya mjini na umeme wake unatakiwa uwe wa TANESCO. Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kata zilizoko kwenye majimbo ya mjini lakini ni kata za vijijini zinapata umeme angalau wa REA ili wananchi hawa waweze nao kunufaika na huduma ya umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba majibu ya uhakika. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Awamu ya Sita inayongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni Serikali sikivu sana. Ninao mpango wa upelekaji wa umeme katika maeneo ya mijini yenye sura ya miji, na mradi huo unaitwa peri-urban. Tayari sasa hivi tangazo limeshatangazwa kwa mikoa minane ya Tanzania Bara kuwapata Wakandarasi watakaopeleka umeme katika maeneo hayo ya peri-urban.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami mwenyewe Jimbo langu la Bukoba Mjini lina maeneo ambayo yanaonekana ni ya mjini lakini yapo vijijini. Kwa hiyo, mradi upo na kabla ya mwaka 2022 kwisha kazi hiyo itakuwa imeanza kufanyika ili kufikisha umeme katika maeneo hayo.
MHE. MASACHE N. KASAKA: Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake hayo. Nami nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Wilaya ya Chunya katika REA Awamu ya Pili tumepata vijiji 12; lakini katika vijiji 12, vijiji 10 vinapita kwenye misitu ambayo iko chini ya TFS. Sasa mradi huu unapopita, TFS imekwamisha huu mradi inasubiri mpaka iweze kupata malipo ya fidia ili mradi uweze kuendelea, kitu ambacho kinashangaza sana.

Je, ni lini sasa Serikali itakaa na taasisi nyingine ya Serikali TFS waweze kujadiliana ili malipo yaweze kufanyika na mradi huu uweze kutekelezeka na wananchi waweze kunufaika kama ambavyo wanategemea? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwenye kila kijiji kitapata transfomer ya KVA 50 ambapo usambazaji wake wake wa umeme ni wastani wa kilometa moja ambayo inahudumia takribani watu 68: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza transfomer yenye ukubwa zaidi ya KVA 50 ili wananchi wengi zaidi waweze kunufaika na huduma hii ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Masache Njelu Kasaka, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kufuatilia masuala ya wananchi na hasa kwenye hili eneo la fidia. Kwanza naishukuru Serikali kwamba ilishirikiana na wananchi na kuwaomba miradi yote ya REA isiwe miradi inayohitaji fidia katika maeneo ambayo miradi inapita. Nawashukuru wananchi kwa niaba ya Serikali walikubali ombi hilo kwa sababu umeme ni kwa mahitaji yetu sote.

Mheshimiwa Spika, kwanza niseme kwamba mradi wa REA hauna fidia kwa wananchi. Ila kwa wenzetu wa TFS wamekuwa wanazo kanuni ambazo zinaelekeza kwamba maeneo yao yakitaka kutumika kwa shughuli nyingine, basi fidia itolewe. Nasi mara kadhaa tumefanya mazungumzo nao ili eneo hili liondoke na kikao cha mwisho kimefanyika wiki hii na tunatarajia kabla ya mwezi huu tutakuwa tumekamilisha jambo hili, ili sasa kama ambavyo tunapeleka miradi ya umeme katika maeneo ya wananchi bila kuwafidia na TFS ambayo ni taasisi ya Serikali pia, isifidiwe kwa kutumia eneo kwa ajili ya shughuli za wananchi. Tuna uhakika jambo hili litakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika awamu hii ya pili eneo la Mbeya lakini pia Katavi, Simiyu na Morogoro yapo maeneo yanahitaji attention ya namna hiyo na tayari tunayafanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye jambo la pili, ni kweli kwamba wateja ambao wamefikishiwa umeme kwa kipindi hiki, siyo wote wanaouhitaji, lakini Serikali imejitahidi sana kwa hizo shilingi trilioni moja na bilioni 250 kupeleka angalau kwa wateja wa awali katika maeneo ya mijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Wabunge wengine wote kwamba Serikali inayo mradi mwingine wa densification ambayo ni jazilizi; inayo mradi mwingine wa Peri-Urban wa kupeleka miradi ya umeme huko na pia TANESCO wanaendelea, kila mtu atapata umeme kwa kadiri Serikali inavyojitahidi kufikisha umeme katika maeneo hayo. (Makofi)
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali la nyongeza katika Wizara hii ya Nishati. Jimbo la Rungwe lina vijiji 99. Katika vijiji 99, vijiji 66 vilikuwa kwenye mradi wa REA II na vijiji 33 viko kwenye mradi wa REA III; lakini katika vijiji 66 ni vijiji 41 tu ndiyo vilikamilishiwa umeme, lakini vijiji 25 havikukamilishiwa umeme katika awamu ya pili ya REA.

Mheshimiwa Spika, Waziri alikuja kufanya ziara kule kwetu kwenye ufunguzi wa REA III tarehe 28 mwezi wa Nane akasema kuna fedha ilibaki kwenye REA II, shilingi bilioni 2.4 kwa ajili ya kupeleka umeme kukamilisha mradi wa umeme kwenye REA II. Akasema, ndani ya miezi miwili huo mradi utakamilika na wananchi watapata umeme.

Mheshimiwa Spika, la kusikitisha, mpaka leo umeme bado haujafika na kazi bado haijaanza. Nilikuwa naomba Waziri atoe kauli hapa, ni lini mradi wa umeme REA II vijiji 25 katika Jimbo la Rungwe utaanza? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mbunge wa Rungwe kwa swali lake. Naomba kutoa majibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye mradi wa REA III round ya kwanza zilikuwepo lots 29 na lots 8 bado hazijakamilika katika eneo hilo la Rungwe na maeneo mengine. Kama tulivyosema, kulikuwa na kuchelewa kwa sababu ya kuchelewa kupatikana kwa vifaa na maeneo kama hayo, lakini Serikali tayari imeiagiza REA kuhakikisha inakamilisha miradi hiyo na wakandarasi kabla ya mwezi wa tatu mwaka huu. Kwa hiyo, vile viporo vyote ambavyo vilibakia kwenye mradi wa REA II, REA III round one, vyote tunatarajia viwe vimekamilika kabla ya kwisha kwa mwezi wa Tatu mwaka huu 2022 eneo la Rungwe likiwemo. (Makofi)
MHE. REHEMA J. MIGILLA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, pamoja na majibu haya mazuri ya Serikali tunaomba yasiishie kwenye maandishi, tunataka kwa vitendo na kwa muda husika, lakini nina maswali madogo mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ilitutangazia bei, hasa sisi watu wa vijijini kwamba, gharama ya kuunganisha umeme ni 27,000/= lakini haikuweka wazi hiyo 27,000/= inajumlisha nini na nini. Sasa tunataka tufahamu;

Je, Serikali inaposema 27,000/= inajumuisha na nguzo bila kuangalia umbali wa mlaji wa mwisho? Kwa sababu, maeneo mengi unalipa 27,000/= lakini hawapelekewi umeme na kila wakiuliza wanaambiwa tatizo ni nguzo, tunataka leo utupe maelezo yanayojitosheleza kuhusu hili tatizo?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili. Kumetokea mabadiliko ya ghafla sana na ya kimyakimya kuhusu bei ya umeme kulingana na units ambazo mnazitoa. Hapo nyuma wananchi walikuwa wakilipa 10,000 wanapata units 78, lakini sasa hivi mabadiliko haya yameasababisha 10,000 hiyo hiyo wanapata unit 28. Sasa je, tunataka tufahamu nini kimesababisha haya mabadiliko ya kimyakimya kwa hizi units ambayo inawatesa sana hawa wananchi wetu ambao ni masikini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rehema, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la kwanza niombe kutoa maelezo mazuri kabisa fasaha kwa niaba ya Serikali kwamba, ukilipa 27,000/= utaletewa umeme ulipo pale kijijini, hata kama ni kwa nguzo 20, ni nguzo moja, ni bila nguzo, maelekezo ya Serikali, gharama ya kuunganisha umeme kwa kijijini ni 27,000/=. Na mara nyingi unapounganisha umeme utahitaji mita, utahitaji nguzo, utahitaji waya, utahitaji transformer pia, ni 27,000/=.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna maeneo ambapo tunapata matatizo Waheshimiwa Wabunge, basi tuwasiliane ilki msimamo huu wa Serikali uweze kutekelezwa katika maeneo ambayo yanahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini katika eneo la pili, kwa taarifa zilizopo, mabadiliko ya bei za umeme ya mwisho yalifanyika mwaka 2016 kwa kanuni zilizotolewa na msimamizi wa bei ambae ni EWURA. Mpaka sasa hatuna taarifa na hatuna maelekezo na hatuna mabadiliko yoyote yale kwenye gharama za umeme. Lakini wale watumiaji wadogo, tunawaita Domestic 1, maarufu D 1, ukiwa na 9,150/= utapata unit 75, lakini kama utatumia zaidi ya unit 75 kwa mwezi unakidhi kutoka kwenye D 1 kwenda T 1 hivyo, 9,150/= haiwezi kununua tena unit 75 unakuwa ume-graduate kwenda kwenye matumizi makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niombe kama kuna Waheshimiwa Wabunge ambao wananchi wao bado wanatumia unit 75 na pungufu kwa mwezi, lakini gharama za ununuzi wa umeme zimebadilika kwao, basi tuwasiliane ili tuweze kubaini tatizo ni nini, tuondoe hilo tatizo, lakini hakuna mabadiliko ya wazi wala ya kimya ya gharama za umeme. Nashukuru.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi, nami niulize swali dogo la nyongeza: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Nkansi ni miongoni mwa wilaya ambazo zinapata umeme kwa muda mfupi sana. Wizara ya Nishati ilisema wanaweza kuondoa tatizo hilo kwa kutuunganisha kwenye gridi ya Taifa kwa hiyo, tunatumia umeme kutoka Zambia.

Nataka kujua kama Wizara bado inaamini mpaka leo kwamba, kuunganishwa kwenye gridi ya Taifa ndio suluhisho, ni lini mtatuunganisha kwenye gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza miradi miwili kwa pamoja ya kupeleka gridi ya Taifa katika Mkoa wa Katavi na Kigoma kwa pamoja. Na gridi hiyo ya Taifa inatarajiwa kufika maeneo hayo ifikapo Oktoba mwaka huu. Na itakapokuwa imefika Katavi ndio sasa tutakamilisha mpaka maeneo mengine ya Jirani ambayo hayana gridi ya Taifa.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini Serikali isiiondoe Wilaya ya Meatu kuchukulia umeme katika Kituo cha Mabuki, Mwanza, chenye umbali wa kilometa 200 ikairejesha Wilaya ya Meatu ilikokuwa mwanzo inachukulia Ibadakuli, Shinyanga, umbali wa kilometa 100 ili kuondoa tatizo la kukatikakatika kwa umeme, ambalo linasababishwa na umeme kusafiri umbali mrefu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kuweka eneo moja kupata umeme kutoka sehemu nyingine ni jambo la kitaalamu na sio kwa kuangalia umbali peke yake, lakini pia na uwezo wa kituo fulani kuhudumia watu wetu walioko jirani, lakini naomba nikiri kwamba, nachukua jambo hilo na nitaenda kuliwasilisha kwa wataalam ili walichakate na kuona kama kwa sasa tunaweza kuhama kutoka upande hu una kwenda kwingine, kwa ajili ya kuboresha huduma hii. (Makofi)
MHE. HASSAN S. MTENGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Mtwara Mjini ni jimbo ambalo kwa sasa linaongoza kwa ukatikaji wa umeme kwa kila siku, mikatiko inaweza ikafika zaidi ya 30 kwa siku. Je, ni lini Serikali itaiingiza Mtwara na Lindi kwenye gridi ya Taifa na sisi tukafaidika na umeme wa gesi ambayo inatoka Mtwara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Mheshimiwa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza niwashukuru wana- Mtwara kwa kuwa, sehemu kubwa sana ya umeme ambayo inalisha nchi hii kwenye gridi ya Taifa inatokea katika Mkoa wa Mtwara. Na nimuahidi kwamba, katika mipango ambayo Serikali ikonayo ni kuhakikisha kwamba, sasa umeme ambao unazalishwa tayari kwenye gridi ya Taifa na kwenyewe uweze kufika. Niseme kwenye mipango tuliyokuwanayo kufikia 2025 itakuwa imefikia hatua sasa ya kuamua ni lini gridi ya Taifa itafika katika Mkoa wa Mtwara na Mkoa wa Lindi kwa ajili ya kufikisha huduma nzuri zaidi.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa, Wilaya ya Ki- TANESCO ya Ukerewe inapata umeme kutoka kwenye kituo cha kupoza umeme kilichoko Bunda, ambako ni umbali mrefu, hali inayosababisha kutokuwa na umeme wa uhakika. Na kwa kuwa Serikali ina mpango wa kujenga vituo kadhaa vya kupoza umeme kwenye maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwa nini sasa Serikali isiweke Ukerewe kama moja ya maeneo ambayo yatajengewa kituo cha kupoza umeme, ili kurahisisha umeme wa uhakika kwenye eneo la Ukerewe? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kulichukua jambo hili, ili wataalam waende wakachakate na kuona economic feasibility ya kuweka kituo pale Ukerewe na uwezo wa kukitumia katika mahitaji tuliyonayo, ili kuweza kuboresha huduma ya umeme katika eneo la Ukerewe.
MHE. NEEMA W. MGAYA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Mimi na Mheshimiwa Festo Sanga tunaishukuru Serikali kwa hatua za awali kuhusiana na bwawa hili, lakini tulikuwa tunataka Serikali ituhakikishie ni lini wananchi wetu watalipwa fidia?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa kuwa wananchi wa Jimbo la Makete wamekuwa na changamoto kubwa sana ya kukatika katika kwa umeme kwa muda mrefu kwa sababu umeme huo unatoka Mbeya.

Je, Serikali inawahakikishia nini wananachi wa Makete kwamba bwawa hili litakuja kuwa tija ya kutatua changamoto hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Neema Mgaya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza baada ya kukamilisha uthamini mwezi Oktoba ndiyo sasa taratibu za malipo zitaanza ikiwa ni kupelekea Mthamini Mkuu wa Serikali na fedha tayari imeshatengwa. Kwa hiyo, baada ya kukamilisha taratibu hizo fedha italipwa, tunaamini kabla ya kufikia mwanzoni mwa mwaka unaokuja wa fedha taratibu zikienda kama zilivyopanga fedha za fidia zitakuwa zinalipwa.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili ni kweli mradi huu ukikamilika utawafaa wananchi wa Mkoa wa Njombe, Wilaya ya Makete, lakini na Watanzania wengine wote kwa sababu ni mradi utakaopeleka umeme kwenye Gridi ya Taifa. Katika kipindi hiki ambacho umeme unakatika katika Serikali imeshafanya tathimini ya kujenga vituo vingine vya kupoza umeme kwenye maeneo mbalimbali na Makete ni eneo mojawapo ambalo limetizamwa kwa ajili ya kuboresha huduma ya umeme.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, ni lini Serikali itajenga kituo cha kupozea umeme pale kwa Mbwembwele ili kuondosha tatizo la kukatikakatika katika Mji wa Handeni?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; mkandarasi anayesambaza umeme wa REA katika Wilaya ya Korogwe, anafanya kazi kwa kusuasua, tangu mkataba ulipoanza mwezi Mei, amesimamisha nguzo katika vijiji vitatu tu. Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusiana na mkandarasi huyu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Ulenge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza Serikali tayari imetoa pesa, shilingi bilioni 500 kwa ajili ya kuimarisha mfumo wa grid ya Taifa na Wilaya ya Handeni ni mojawapo ya eneo ambapo patajengwa kituo cha kupooza umeme katika eneo la Mkata kwa kuanzia na kinajengwa mwaka huu wa fedha wa 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili, mkandarasi anayepeleka umeme vijijini katika eneo la Korogwe, tutahakikisha kwamba kufikia Desemba mwaka huu anakamilisha kazi kwa sababu ndiyo mujibu wa mkataba. Tunaendelea pia kufuatilia kwa karibu kuondoa zile changamoto ndogo ndogo ambazo zilikuwa zimejitokeza za upungufu na ukosefu wa vifaa lakini kazi zitakamilika kwa wakati.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Spika, ahsante, je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vitongoji 42 vilivyobakia katika Jimbo la Kalenga, Mkoani Iringa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, Iringa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kupeleka umeme katika vitongoji vyote nchini kwa jinsi upatikanaji wa fedha unavyoendelea. Hatua ambayo tunaendelea nayo sasa ambayo inatakiwa kukamilika ni hatua ya vijiji ambayo itakamilika Desemba mwaka huu na fedha zinavyozidi kupatikana, vitongoji vinapelekewa pia umeme.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Je, ni lini Serikali itakamilisha usambazaji wa umeme katika vijiji vya Kata ya Kiru na Magara, Jimbo la Babati Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, umeme vijijini katika eneo alilolitaja utakamilika mwezi Desemba, Mkandarasi wa Giza Cable Industries Limited ambaye anapeleka umeme katika Mkoa wa Manyara, anaendelea na kazi na tutaendelea kusukumana naye ili akamilishe kazi kwa wakati.
MHE. MICHAEL C. MWAKAMO: Mheshimiwa Spika, mkandarasi anayepeleka umeme Kibaha Vijijini kwenye Kijiji cha Kimaramisale, tulikubaliana afike site kwa maelezo yake mwezi wa Sita na mpaka sasa hajafika. Je, ni nini kauli ya Serikali kwa mkandarasi huyu ili akamalizie kazi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Michael, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wakandarasi wote wa REA wako katika maeneo yao ya kazi mbalimbali. Unakuta mkandarasi mmoja katika mkoa mmoja labda ana wilaya nne au tano na tulipunguza kazi. Naomba nieleze kwamba baada ya hapa nitalifuatilia jambo hili kujua kwa nini mkandarasi huyu hajafika na kama amefika maeneo mengine basi ni lini atafika katika eneo la Mheshimiwa Mbunge alilouliza.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Katika Kitongoji cha Ngana katika Wilaya ya Rungwe kina kaya 600, lakini waliowekewa umeme wa REA ni kaya 32 peke yake. Serikali haioni interval ni kubwa sana na ni lini itaweza kupeleka umeme katika eneo lile?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sophia Mwakagenda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, maendeleo ni hatua na nia ya Serikali ni kuhakikisha kila mwananchi mahali popote alipo anafikiwa na umeme. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali inaendelea kupeleka umeme kwenye maeneo ya vijiji na vitongoji na kila mwananchi atafikiwa kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ahadi ya Wizara ya Nishati kwa kituo hiki cha kupoza umeme ambacho kinatarajiwa kujengwa kwenye Kata ya Mbutu iliyopo Jimbo la Igunga ilikuwa ifanyike kwa mwaka huu wa fedha, lakini naona Serikali wameamua kuisogeza tena mwakani; ukiangalia imekuwa na changamoto kubwa kwa sababu tunapata umeme kutoka Lusu, Nzega ambayo ni kilometa 100. Sasa je, Serikali haioni kuchelewa kujenga kituo hiki ni kudumaza uchumi wa wananchi wa Jimbo la Igunga?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Ngassa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatilaji wake wa mara kwa mara. Ni kweli Serikali ilikuwa imetoa ahadi ya kukijenga kituo hiki, lakini mwaka 2021 na mwaka huu wa fedha 2022/2023, Serikali kupitia TANESCO imefanya upembuzi yakinifu katika maeneo yote Tanzania Bara kuona uhitaji halisi wa ujenzi wa vituo vya kupooza umeme.

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu niseme kwamba upembuzi yakinifu ulipokamilika, tukabaini mahitaji kutoka maeneo mbalimbali na uhitaji wa haraka zaidi kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. Kwa hiyo, Kituo cha Igunga hakijachelewa ila imeonekana kijengwe mwakani kwa sababu kuna wenye uhitaji mkubwa zaidi kwa mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, naomba uniruhusu nivitaje vile vituo ambavyo vitajengwa mwaka huu ambavyo tayari vimepatiwa fedha katika ule mradi wetu wa grid stabilization project.
MHE. ASSA N. MAKANIKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa muktadha wa hali ya umeme ya Igunga, Julai 19, Mheshimiwa Waziri akiwa Biharamulo alieleza kwamba mnamo mwezi Septemba umeme wa gridi ya Taifa utakuwa umefika Kigoma. Sasa tupo mwezi Septemba, tunataka kujua hali ya umeme wa gridi ya Taifa: Je, umeshawasili Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Assa Makanika, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, umeme wa gridi utafika Mkoani Kigoma mwezi huu Septemba kwa sababu ipo njia ya msongo kV 33 ambayo inakamilishwa mwishoni mwa mwezi huu inayotokea Nyakanazi kupita Kakonko – Kibondo Kwenda mpaka Kasulu. Kwa hiyo, umeme wa gridi kwa kuanzia utaingia mwezi Septemba katika Mkoa wetu wa Kigoma.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kumekuwa na changamoto ya katikakatika ya umeme katika Jimbo la Igalula lakini ukiuliza, unaambiwa changamoto hiyo inasababishwa na kusafiri kwa umbali mrefu wa nishati hii ya umeme: Je, Serikali haioni haja ya kujenga vituo vya kupoozea umeme katika Kata ya Kigwa na Kizengi ili kupunguza adha ya kusafiri umeme na kupunguza changamoto ya katikakatika hii ya umeme?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika huu mpango wa grid stabilization project kwa mwaka huu wa fedha, Tabora inavyo vituo viwili vya kupooza umeme ambacho kitajengwa pale Uhuru katika Wilaya ya Urambo na kingine kitajengwa Ipole katika Wilaya ya Sikonge. Kwa Mheshimiwa Venant kule Igalula nitaenda kuangalia kwenye mpango wetu wa ujenzi wa vituo vya kupooza umeme katika wilaya zenye mahitaji na nitamfahamisha ni lini Serikali imejipanga kukijenga katika eneo lake. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza namshukuru Mheshimiwa Waziri kwmaba amekitaja kituo cha kupoozea umeme Urambo: Je, anawahakikishiaje wananchi wa Urambo kwamba lini kituo hicho kinakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Margaret Sitta, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Margaret Sitta na wananchi wa Jimbo lake kwamba katika mwaka huu wa fedha 2022/2023 kutoka katika Shilingi bilioni 500 ambazo zimewekwa kwa ajili ya uendelezaji wa gridi, vile vituo 15 vitakavyojengwa, na cha kwake cha pale Uhuru kitakamilika bila matatizo yoyote.
MHE. ABEID R. IGHONDO: Mheshimiwa Spika, ninakushukuru kwa kunipatia fursa. Pamoja na majibu haya ya Serikali ningeomba kujua, kwa kuwa mradi huu ni muhimu sana katika nchi yetu, pia umechukuwa muda mrefu sana bila kukamilika. Je, Serikali sasa ina mkakati gani mahsusi na wa ziada wa kuhakikisha mradi huu unaanza uzalishaji mara moja. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani, Mbunge wa Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama tulivyosema Mkandarasi tayari amepatikana kwa ajili ya majadiliano lakini tumepata changamoto ndogo ya yeye kuhitaji vitu ambavyo havikuwemo kwenye masharti ya tenda ya zabuni. Tumeshafikia mwisho na msimamo wa Serikali ni kwamba hakutakuwepo na Government Guarantee kwenye mradi huu, bali akubaliane tufanye vile tulivyokubaliana tangu mwanzo.

Mheshimiwa Spika, akikubali Januari tutaanza kufanya kazi hii na asipokubali, Serikali sasa ishaamua kuendelea mbele na Zabuni hii mpya ili tuweze kuhakikisha tunampata Mkandarasi wa kufanya kazi hii kwa wakati. (Makofi)
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kyerwa tuna Vitongoji 670, Vitongoji ambavyo vina umeme ni vitongoji 170, vitongoji 500 vyote havina umeme sawa sawa na asilimia zaidi ya 75.

Je, nini mkakati wa Serikali wa kupelekea vitongoji vingine ambavyo havina umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la Pili; Mkoa wa Kagera ni miongoni mwa Mikoa ambayo tunapata adha kutokana na umeme unaokatika mara kwa mara. Je, nini mkakati wa Serikali wa haraka kuunganisha Mkoa wa Kagera na gridi ya Taifa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali wa kupeleka umeme katika maeneo ya vitongoji ni katika maeneo matatu. Kwanza ndiyo hii ambayo tunaifanya saa hizi ya REA III Round II, ambayo inafikisha umeme katika vijiji lakini katika vitongoji pia. Kama tulivyosema kwenye jibu la misingi Vitongoji 33 vitapata umeme.

Mheshimwa Spika, kuna mkakati wa pili ambao unafanyika wa umeme jazilizi (densification) na Mkoa wa Kagera kwenye eneo lake la Kyerwa densification katika two B na C zimo na kuanzia Januari tutaongeza wigo wa kupeleka kwenye maeneo hayo.

Mheshimwa Spika, Serikali inaendelea kutafuta pesa sasa nyingi zaidi kwa ajili ya kumaliza vitongoji vyote nchini takribani kama elfu 30 na zaidi ambavyo havijapata umeme, inahitajika karibia Trilioni Sita na Bilioni Mia Tano kuweza kukamilisha eneo hili lote na jitihada za Serikali kutafuta hizo pesa zinaendelea.

Mheshimiwa Spika, kuhusu swali la pili, mwezi huu, Mheshimiwa Rais amezindua kituo cha kupooza umeme cha pale Nyakanazi ambacho ndiyo sasa kimeingiza Gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma na katika Wilaya mbili za Mkoa wa Kagera ambapo ni Ngara na Biharamulo. Jitahada za kuhakikisha kwamba Mkoa mzima wa Kagera unapata umeme kutoka katika chanzo hicho unaendelea na tayari mradi wa kuanza kupeleka umeme kutoka Benako kwenda Kyaka umeshatangazwa na Mkandarasi anatafutwa ili sasa Mkoa wa Kagera na wenyewe uweze kuingia katika Gridi ya Taifa hivi karibuni.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo la Hai maeneo mengi yamekuwa na miundombinu ya umeme ambayo ni chakavu sana, jambo ambalo ni hatari. Katika Kata ya Uroki, Masama Kusini, Machame na maeneo mengi yamekuwa na miundombinu ambayo kwa kweli ni chakavu sana. Tuliwasilisha maombi maalum ya kupewa vifaa kwa ajili ya kufanya marekebisho.

Je, ni lini Serikali itatuletea vifaa hivi ili kutuondoa kwenye hatari ya miundombinu ambayo imekuwa chakavu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Mafuwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kurasimisha na kurekebisha miundombinu yake ya umeme inayowapelekea wananchi nishati hiyo. Katika Mwaka huu wa Fedha, Serikali imetenga jumla ya Shilingi Bilioni 500 kwa ajili ya kurekebisha Gridi ya Taifa katika maeneo ya umeme mkubwa pia imetenga Bilioni 300 kwa ajili ya kurekebisha miundombinu ya umeme kwenye maeneo madogo madogo ambayo tunaziita ni project mapato.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba na yeye atapata mgao huo kwa ajili ya kurekebisha miundombinu yake chakavu ili huduma hii iweze kuendelea kupatikana katika eneo lake la Hai. (Makofi)
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Mkoa wa Rukwa, Wilaya ya Sumbawanga Mjini, Kata ya Malangali, TANESCO waliweka kipooza umeme kwenye Kata hiyo.

Je, ni lini sasa Serikali itawalipa wananchi wa kule fidia? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Bupe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ninaomba nikimaliza maswali nikapate eneo maalum, eneo ni eneo gani na fidia ni fidia gani ili niweze kulishughulikia na kujua kwa nini halijafanyiwa kazi kama changamoto hiyo bado ipo.
MHE. BENAYA L. KAPINGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ninaishukuru Serikali kwa majibu mazuri, nina swali moja la nyongeza lenye sehemeu (A) na (B).

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa lane iliyopo sasa ni hiyo ambayo inayotumika Songea, inatumika Mbinga pia inatumika Nyasa. Kwa kuwa kuna ongezeko kubwa sana la utumiaji wa umeme kutokana na uchimbaji mkubwa wa makaa ya mawe pale Mbinga, viwanda vikubwa vya kubangua kahawa, viwanda vya kusaga sembe na viwanda vya maji ni vingi hali inayopelekea umeme kuwa wa low voltage au kukatikakatika.

Je, Serikali iko tayari kurudisha mpango wake nyuma badala ya mwaka 2024/2025 uwe 2023/2024 ili kuwafanya wananchi nao wapate nafasi ya kutumia umeme ambao sasa haukatikikatiki.

Mheshimiwa Spika, ikiwa hili haliwezekani, je, Serikali itaisaidiaje Mbinga kuondokana na hali hii ya kukatika katika kwa umeme?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza lililoulizwa na Mheshimiwa Benaya Kapinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikweli kwamba Mkoa wa Ruvuma umekuwa na changamoto ya maeneo kuwa na matatizo ya low voltage, na kwa sasa kwenye bajeti ya mwaka huu, kama tulivyosema tumeiweka Mbinga, kuna line ya kujengwa inayotoka Songea kwenda Tunduru ambayo ina kilometa kama 211. Serikali ilifanya uhakiki wa matatizo na ikagundua kwamba hapo kuna changamoto kubwa zaidi, na wako wale wenye changamoto kidogo na ambao hawana changamoto zaidi. Kwa hiyo eneo la Mbinga limewekwa kwenye wale wasiokuwa na changamoto sana kama hao wengine.

Mheshimiwa Spika, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali itaendelea kuifanyia marekebisho na matengenezo ya mara kwa mara hii line ya kutoka Songea kwenda Mbinga na tuone uwezekano wa kuivuta mapema kabla ya ule muda uliopangwa kulingana na bajeti itakavyokuwa imewekwa.
MHE. ENG. SAMWELI X. HHAYUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Wilaya ya Hanang tunachangamoto kubwa sana ya umeme kukatika mara kwa mara, na suluhu ya tatizo hili ni kujengwa kwa kituo cha kupooza umeme pale Mogitu. Serikali iliahidi kutoa zaidi ya shilingi bilioni mbili ili ujenzi huo ufanyike.

Je ujenzi huo utaanza lini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hhayuma kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kujibu kwenye maswali mengine, Serikali imefanya utafiti na kubaini maeneo yanayohitaji kujengwa vituo vya kupooza umeme kwa ajili ya kuhakikisha huduma inawafikia wananchi, na eneo hilo ni mojawapo kati ya maeneo ambayo yametengewa na muda utakapofika huduma hiyo itatekelezwa kwenye jimbo lake.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika mgogoro huu wa madai ya fidia, hivi sasa umechukua miaka mitano na jumla ya watu 63 wamehusishwa katika jambo hili: Je, Serikali ipo tayari kulipa fidia ya nyongeza kutokana na ucheleweshaji wa malipo haya?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, napenda kutaka kujua: Je, ni lini Mheshimiwa Waziri atakuwa na nafasi ya kuweza kuambatana nami twende kwa pamoja tukasuluhishe huu mgogoro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nianze na la pili, tukimaliza kipindi hiki cha Bunge, tutapanga ratiba vizuri na Mheshimiwa ili tuweze kuona namna ya kumaliza jambo hili kwa pamoja kwa ajili ya kuwahudumia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza, Serikali ipo tayari kumlipa mtu fidia kwa kadri anavyostahili kwa mujibu wa sheria. Kwa hiyo, kama nilivyosema, tutaenda pamoja na kusaidiana kutatua jambo hili, na lipatakapokwisha wale wanaostahili kulipwa fidia na kwa mazingira tuliyokuwa nayo, aidha ya ucheleweshaji au nyongeza, itafanyika kwa mujibu wa sheria.
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lakini kumekuwa na uendelezaji mdogo sana wa miradi ya REA iliyopo kwenye Majimbo yote ya Mkoa wa Mtwara.

Swali la kwanza; pamoja na mikakati hii ya Serikali ya kutaka kuimarisha upatikanaji wa umeme kwenye wilaya zetu, ni lini sasa tutahakikisha Miradi ya REA iliyopo kwenye Majimbo yote ya Mkoa wa Mtwara inakamilika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; tunataka kufahamu kwa uhakika kwa sababu mpaka sasa kuna vijiji zaidi ya 300 havijapatiwa umeme, wanaleta umeme wa grid kutoka Mtwara na hii wanayosema kutoka Mombika ili kuimarisha upatikanaji wa umeme kwenye Wilaya ya Masasi, nayo tunaomba kufahamu miradi hii itaanza kutekelezwa lini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Cecil Mwambe kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mikataba mingi ya REA III, round two ilikuwa inatakiwa kuisha Desemba, lakini kwa changamoto ambazo zilijitokeza ambazo tayari tulishazisema, muda wake wa kukamilika utaongezeka kidogo kulingana tofauti tofauti ya maeneo. Hata hivyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote kwamba Serikali kupitia Wizara ya Nishati inahakikisha kwamba mikataba hii inakamilika na wananchi wanapata umeme katika vijiji vyao, kwa sababu pesa ipo na usimamizi unaendelea kufanyika wa karibu. Kwa hiyo, tutaendelea kulisimamia hili ili umeme uweze kupatikana katika maeneo yetu.
MHE. ALLY M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni miezi mitatu sasa katika Wilaya ya Kyela, umeme haupatikani mchana. Je, ni lini wananchi wa Kyela watajisikia kwamba nao wana haki ya kupata umeme asubuhi na mchana?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ally Jumbe, Mbunge wa Kyela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba baada ya hapa nikafuatilie ili kufahamu kwa nini Mheshimiwa Mbunge katika jimbo lake kwa miezi mitatu hakupatikani umeme mchana. Ninachofahamu ni kwamba kwa sababu ya upungufu wa umeme kumekuwa na kupungua kwa umeme kwenye baadhi ya maeneo, lakini jambo la kwamba miezi mitatu mchana wote hakuna, hilo ni jambo la kufuatilia, halafu tutashirikiana na Mheshimiwa Mbunge ili tuweze kutatua changamoto hiyo.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona. Naomba Serikali ituambie hususani Wizara ya Nishati, kuna kigugumizi gani hasa katika suala la REA? Maana yake kumekuwa na changamoto kubwa sana kwa hawa Wakandarasi hawatoi ushirikiano, lakini hawashughuliki kabisa na miradi ile inayotakiwa ifanyike kule. Mfano kwenye jimbo langu ule mkataba uliopita haujatekelezwa hata katika kijiji kimoja. Sasa Serikali ina kigugumizi gani katika jambo hili, ituambie ukweli?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mchungahela, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, niombe kupata ushirikiano wa Waheshimiwa Wabunge kwa sababu ni case by case kwamba Mkandarasi hana ushirikiano mzuri na Mbunge. Wako Waheshimiwa Wabunge wengine ambao wanatoa sifa nzuri na recommendation nzuri kwa wakandarasi waliokuwa nao kwamba wanatoa ushirikiano. Kwa hiyo, naomba kwa wale ambao wanapata changamoto ya ushirikiano, basi tuwasiliane ili tuweze kutatua changamoto hizo katika maeneo yao ili tuweze kuhakikisha kwamba miradi hii inakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo lingine, tuwasiliane pia na kupeana taarifa na updates sahihi za ni lini umeme umewaka wapi na utawashwa wapi na pale ambapo tunaona kuna changamoto za ucheleweshaji usiokuwa na sababu kwa pamoja tuweze kushirikiana na kuchukua hatua ili tufikie azma ya kuwasha umeme katika vijiji vyetu vyote kwa kadri ya mikataba, lakini na lengo la Serikali Awamu ya Sita inaongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza kuhusu suala la Mkandarasi wa REA katika Mkoa wetu wa Songwe. Nafikiri hili tatizo Waziri analifahamu na binafsi nimekwenda ofisini kwake mara kadhaa kuhusu huyo Mkandarasi. Kwa kifupi huyu mkandarasi ana kiburi, mpaka sasa hivi amewasha vijiji vitano tu mkoa mzima na ana majibu ya jeuri, Waziri mwenyewe ameshuhudia. Sasa nini mkakati wa Wizara au Waziri yuko tayari kwenda Songwe kuonana na huyu mkandarasi kuhusu tatizo la REA, Mkoa wa Songwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwenisongole, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkandarasi anayetekeleza mradi wa REA III, Round Two katika Mkoa wa Songwe, ni mkandarasi anayeitwa Derm Electric ambaye pia anafanya kazi hiyo katika Mkoa wa Dodoma. Mkandarasi huyu siyo hohehahe, siyo legelege, ni mojawapo ya wakandarasi ambao tunawatarajia wafanye kazi nzuri. Changamoto ambayo Mheshimiwa Mbunge ameisema tumeshaanza kuifanyia kazi na tutaendelea kusukumana na kusimamiana ili kazi hizo zote za maeneo husika ziweke kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, tayari tumeshapanga kikao na wakandarasi hawa, mwishoni mwa mwezi huu ili tuweze kwa pamoja changamoto ambazo zinatokea kwa upande wao ili tuweze kuzitatua na kuhakikisha miradi inakamilika kwa wakati.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, naungana na Wabunge wenzangu, mkandarasi ambaye amepewa Miradi ya REA katika Wilaya za Mvomero, Ulanga, Malinyi, Kilosa mpaka sasa hajawasha umeme katika kijiji hata kimoja. Sasa na hilo nalo wananchi wa Jimbo la Mikumi wanataka kujua nini kauli ya Serikali kwenye hili?

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba baada ya hapa niwasiliane naye ili nijue changamoto hasa kwenye eneo lake ni sehemu gani anasema hakujawasha hata kijiji kimoja. Baada ya hapo tutafuatilia kujua changamoto iko wapi, pengine ni kwa sababu mkandarasi anakuwa na maeneo manne, matano, sita pengine kaanzia kwingine kwake hajafika. Zile hatua za awali za kuhakiki mipaka, kuhakiki maeneo ya kuweka miundombinu na kuhakiki urefu, tayari zimeshafanyika kwenye maeneo yote inafuata kuweka nguzo, kuvuta wires na sasa kuwasha umeme. Kwa hiyo, tukishafuatilia tutajua hatua gani imefikiwa katika eneo lake, lakini kazi hiyo lazima ifanyike na kukamilika.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Naishukuru Serikali kwa sababu wakati natoa swali hili nilikuwa na mahitaji ya kata mbili zenye mitaa zaidi ya 14, yenye sura za vijiji. Sasa hivi ninavyozungumza Kata za Lwanima na Kishiri, mkandarasi wa REA, kwa gharama ile ile ya Shilingi 27,000/= anaendelea kufanya kazi na wananchi wangu wanafurahia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naishukuru sana Serikali. Nitoe tu msisitizo uchambuzi huo utakapokamilika utatusaidia kujaziliza maeneo ambayo yatakuwa yamebaki kwa gharama nafuu kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kupokea pongezi na maombi ya Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa yamagana na kwamba tunashukuru ameona Serikali inavyojitahidi kuendelea kutekeleza huduma hii ya kupeleka umeme kwa wananchi kwa gharama nafuu.

Mheshimiwa Spika, hili la kukamilisha zoezi la utambuzi wa maeneo kama tulivyojibu kwenye swali la msingi, tutahakikisha linakamilika kwa wakati na liweze kutusaidia katika maeneo yetu sote.

Mheshimiwa Spika, nami Jimbo langu la Bukoba Mjini likiwemo linafanana na la kwake pia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi. Naomba tu nimwulize Mheshimiwa Naibu Waziri; tulileta malalamiko kuhusu hii miji midogo ambayo ina sura ya vijiji, mkasema tathmini inafanyika na hiyo timu itakuja kwa Wabunge ili tufahamu kama mnafika maeneo yetu. Sasa ni lini hii timu yenu itafika kwa Wabunge hawa? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Olelekaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli, tuliahidi kwamba kuna timu itaenda kuwatembelea na kuzungumza na Wabunge ili kuweza kubaini yale maeneo ambayo tunataka kuyafanyia kazi. Timu hii imeanza kufanya kazi ya ndani, ni kama ku-plot maeneo ambayo inatakiwa iende kuyatembelea kwa sababu kuna mengine yanafahamika, hayahitaji kwenda kukaguliwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hii shughuli ya ndani ya utambuzi itakapokuwa imekamilika kwa taarifa iliyokuwepo, ndiyo sasa itaenda site na Waheshimiwa Wabunge wote wanaohusika wataiona hii timu kwa sababu maelekezo ya Wizara ndivyo yalivyo kwa ajili ya kushirikiana kuweza kutambua maeneo hayo kwa usahihi zaidi. Ahsante sana.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, swali langu la msingi nimeomba kupatiwa vifaa kingaradi kwenye eneo la Mwese.

Je, Serikali ni lini itapeleka hivyo vifaa kwa kuwa, eneo hilo lina radi za mara kwa mara na wananchi wengi wamekuwa wakipoteza maisha yao na mali zao, hasa mifugo?

Mheshimiwa Spika, napenda kupata majibu ya msingi kwa Mheshimiwa Naibu Waziri atueleze vifaa hivyo vitafika lini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Kakoso, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa sababu utekelezaji wa bajeti ya mwaka 2022/2023 bado unaendelea na sasa tuko katika robo ya pili, namhakikishia Mheshimiwa mbunge kwamba tutahakikisha hii pesa imeenda na kwenye maeneo hayo ya Mwese pia, vifaa hivi vitafika kwa kukamilisha na hiyo miundombinu ya umeme ambayo inahitajika katika maeneo hayo kwa haraka iwezekanavyo.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwanza napongeze jitihada zinazoendelea kwa upande wa Serikali, lakini changamoto mojawapo inayofanya matumizi ya gesi kuwa yapo chini zaidi ni kukosekana kwa vituo vya kuuzia gesi, hasa katika maeneo ya vijijini ambayo yapo mbali na yanasabababisha kuongeza gharama kubwa kwenye mitungi pomoja na gesi kwa ujumla.

Je, Serikali ina mpango gani wa kurekebisha hali hiyo?

Jambo la pili, sambamba na gesi umezungumzia kuhusu kuwezesha nishati safi katika maeneo ya vijijini, bado maeneo ya vitongoji ambavyo ni vikubwa sana havijapata nishati safi ya umeme, Serikali ina mpango gani wa kuharakisha kufikisha nishati hiyo, sambamba na hii ya gesi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Manyanya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la kwanza, wakati wa utekelezaji wa huu mradi wa kutoa ruzuku, tunaamini wigo wa wafanyaji biashara kwenye eneo hili wataongeza na hivyo watafika katika maeneo yote kwa sababu Serikali itajitahidi kuhakikisha shughuli hii inapata ruzuku na hivyo wawekezaji mbalimbali wanaweza kushiriki. Pia, mwongozo tunaoutengeneza utaangalia namna ya kufanya, kama wanavofanya wenzetu wanaosambaza mbolea na maeneo kama hayo, ili tuweze kufika katika maeneo yote husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini, kwenye swali la pili la umeme wa vitongoji, Serikali inaendelea katika mzunguko wa tatu awamu ya pili ya REA, viitongoji baadhi vinapatiwa umeme, lakini pia kuna miradi ya jazilizi inaendelea katika maeneo yetu na Serikali inaendelea kutafuta fedha kuhakikisha kwamba vitongoji vyote vinapatiwa umeme ili wananchi waweze kutumia nishati hiyo safi.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, ni hatua zipi zimefikiwa katika ujenzi wa njia ya msongo wa Kilovoti 132 inayotokea Mkata kupita Handeni Mjini kwenda Kilindi?

Swali la pili, Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kuwa kukatikakatika kwa umeme na kutokuwa na umeme unaokidhi ndani ya Wilaya ya Handeni kumesababisha shughuli za uzalishaji kusimama na hasa kwenye migodi mikubwa iliyopo ndani ya Wilaya.

Je, uko tayari kuambatana na mimi baada ya Bunge hili ukaione hali halisi ya jinsi ambavyo uzalishaji umesimama kwenye viwanda vyetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Reuben Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua iliyofikiwa sasa katika utaratibu wa kujenga njia ya Mkata kwenda Kilindi kupitia Kwambwembwele, Handeni Mjini ipo katika utaratibu wa zabuni. Tunatarajia mwishoni mwa mwaka huu mkandarasi wa eneo hili na maeneo mengine ambapo tutajenga vituo vya kupooza umeme na line za kusafirisha umeme watakuwa wamepatikana. kwa hiyo saa hivi hatua ni ya zabuni na tayari maombi yameshafanyika inaendelea evaluation kwenye maeneo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili, nipo tayari kabisa kuambatana na Mheshimiwa Mbunge kwenda Handeni Mjini lakini pia na maeneo mengine yenye matatizo ya namna hii ili tujionee na tuweze kuweka msukumo katika utekelezaji wa maelekezo na ahadi za Serikali kwa wananchi. (Makofi)
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu kwamba nasikitishwa na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, mradi huu toka mwaka 2016 Mheshimiwa Waziri aliekuwepo alisema 2017 utekelezaji utaanza na utakamilika 2019 leo tunaambiwa mpaka 2027, nataka kujua sababu kubwa ya mradi huu kusuasua na hizi danadana inatokana na nini?

Swali la pili, najua kwamba kulikuwa kuna majadiliano kati ya Serikali na Benki ya Exim ya China kwa ajili ya mkopo wa Dola Milioni 132. Nataka kujua majadiliano haya yamefikia wapi ili mradi huu uweze kutekelezwa na wananchi wa Mkoa wa Singida tumechoka kudanganywa. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Jesca kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimetaja miradi mitatu iliyopo katika Mkoa wa Singida sasa sijui alitaka kujua upi kati ya hiyo lakini kwa swali la pili ninaamini alitaka kujua mradi ambao unatekelezwa kati ya Mkandarasi anayeitwa GEO Wind ambaye kwa sasa financier wake ni Green Climate Fund.

Mheshimiwa Spika, miradi hii kama tulivyosema inatekelezwa na wawekezaji binafsi, Serikali tunaweka mazingira ya uwekezaji baada ya hapo yeye anatakiwa atafute mfadhili atakayeweza kumfadhili na kukamilisha eneo lake la uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, mwenzetu wa GEO Wind huyu ni mfadhili wake wa tatu, alienda Exim wakajadiliana lakini hawakukubaliana baadaye akapata mtu mmoja anaitwa Aplonia kutoka Hispania wakajadiliana hawakukubaliana, sasa saa hizi yupo na huyo ambaye tunamuita Green Climate Fund wanaendelea na majadiliano, watakapokamilisha na wakawa tayari kuwekeza upande wetu tumeshakamilisha, tumeshaweka masharti na tuko tayari kumpokea kwa ajili ya uwekezaji.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana tukasema tunatarajia kati ya mwaka 2023 mpaka 2027 miradi hii itakuwa imekamilika baada ya kukamilisha upande wao.
MHE. MUSSA R. SIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru nami niungane na Dada yangu Jesca Kishoa jambo hili limekuwa la muda mrefu sana.

Mheshimiwa Spika, nataka nimwombe Mheshimiwa Waziri kama atakuwa tayari yeye pamoja na hao wawekezaji GEO Wind na wengine tukutane kwa pamoja kabla Bunge hili halijaisha ili kuweza kujadili mstakabali wa mradi huu wa umeme wa upepo pale Singida Mjini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sima la nyongeza kwamba Wizara tuko tayari kufanya jambo hilo kwa maslahi ya wananchi wa Singida na Watanzania kwa ujumla.
MHE. HAWA S MWAIFUNGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nisikitike sana sijui kama swali langu lilieleweka vizuri kwa sababu mimi nilitaka kufahamu kwa nini umeme unakatika katika kwenye maeneo ya biashara, sikutaka kujua kwanini umeme unakatika kwenye nchi nzima kwa sababu najua tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo ningetamani kufahamu nini mkakati wa Serikali kuacha maeneo ya biashara nyakati za mchana yaweze kufanya kazi kwa kutokukata umeme na umeme huo wakakata nyakati za jioni ili kama kuna matengenezo yoyote yaweze kuendelea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili, umeme umekuwa ukikatika mara tano kwa siku katika siku saba katika Soko la Kariakoo, sehemu ambayo wafanyabiashara wengi wamekuwa wakifanya biashara zao. Je, Serikali ina mpango gani wa kuondoa mgao wa umeme katika Soko la Kariakoo na maeneo mengine ya biashara wakati wa mchana ili watu waweze kufanya biashara zao na usiku waendelee na utaratibu wao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza yla Mheshimiwa Mwaifunga, kama ifuatavyo: -

Mwenyekiti Mheshimiwa, nianze na la kwanza la jumla kwamba umeme unapokatika hauchagui sehemu za kukatika kwa sababu njia inakuwa ni ndefu sana. Hata hivyo, kwa sababu Serikali inafahamu kuna changamoto hiyo, ndio sasa imetengeneza huu mradi ambao unakwena kuondoa matatizo ya ukatikaji wa umeme katika maeneo yote nchini. Hata hivyo kwa umaalum wa maeneo ya biashara kama ambavyo Mheshimiwa Mwaifunga amesema, Mwezi Februari katikati mbele ya Mheshimiwa Rais tunatarajia kusaini miradi ya kupeleka umeme kwenye maeneo maalum ya kibiashara ambayo imeanzishwa project inayoitwa Project Mapato katika Shirika letu la TANESCO na ikilenga hasa kwenye maeneo haya hasa ya kibiashara ili yapate umeme wa uhakika muda wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa umahsusi wa soko letu la Kariakoo, nimweleze Mheshimiwa Mbunge kwamba soko la Kariakoo linapokea umeme kutoka kwenye Vituo vya Kupooza Umeme vinne, vya Ilala, Posta, Mnazi mmoja na Station na inapokea umeme kwa njia za kuleta umeme tunazoziita feeders 13 kutoka kwenye haya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia ilikuwa ni kuhakikisha kwamba haya maeneo yanasaidiana katika kupeleka umeme kwenye eneo hili. Ni kweli kwamba eneo la Kariakoo linapata shida ya umeme mara kwa mara lakini ni kwa sababu ya shughuli ambazo zinaongezeka pale na pengine tunakuwa hatuna taarifa. Hata hivyo, tulichokubaliana ni kuongeza uwezo wa transformer zilizoko kwenye eneo lile ili kuhakikisha kwamba umeme unapatikana muda mwingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kugawana umeme huyu apate mchana, huyu apate usiku ni kulingana na maeneo ya uhitaji. Kwa sababu kuna maeneo mengine ya biashara yanahitaji umeme mchana na kuna maeneo mengine yanahitaji usiku na pengine muda wote. Ninachoweza kuwahahikishia Waheshimiwa Wabunge ni kwamba Serikali imejipanga kuhakikisha meneo yote ya kibiashara yanapata dedicated lines maalum kwa ajili ya kuhakikisha umeme unapatikana muda wote katika maeneo hayo. Hivyo hilo litafanyika kupitia Project Mapato lakini na TANESCO itaendelea kulitazama eneo la kariakoo kama eneo maalumu la kimkakati kwa ajili ya kuhakikisha umeme unapatikana muda wote. (Makofi)
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Ngara. Jimbo la Ngara ni miongoni mwa majimbo ambayo bado yana kata hazijawahi kuona hata nguzo moja ya umeme. Mathalan kata ya Bugarama, Keza, Kibogora pamoja na Muganza wananchi hawa hawajafikiwa na miundombinu ya umeme. Naomba sasa kuiuliza Serikali, je, ni lini wananchi wangu hawa watapelekewa huduma ya umeme? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Jimbo la Ngara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote ya kata na vijiji ambayo hayajapata umeme yako katika mpango wa REA awamu ya tatu, mzunguko wa pili ya upelekaji wa umeme katika maeneo hayo na mradi huo tunatarajia mwishoni mwa mwaka huu uwe umekamilika. Ni kweli kuna maeneo yamesuasua kwa muda mrefu katika upelekaji wa umeme na Mkoa wa Kagera ikiwa ni mmojawapo. Tumechukua jitihada za makusudi za kukaa na Wakandarasi hao na kuwasimamia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika muda mfupi sana ataona Wakandarasi wakirudi kwenye maeneo hayo kuweza kufanya kazi na kutimiza ndani ya muda na tulipeana hadi muda mfupi wa miezi mitatu kuhakikisha maeneo ambayo hayajafikiwa kabisa sasa miundombinu imefika. Kwa hiyo tutapeana taarifa na Mheshimiwa Mbunge ya ufikaji wa Mkandarasi kwenye maeneo hayo na utekelezaji wa mradi kwa mujibu wa mkataba.
MHE. KUNTI Y MAJALA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ili niweze kuuliza swali la nyongeza. Kwa kuwa Serikali imekiri kwamba kuna changamoto kubwa ya umeme nchini lakini wamekuwa wakikata umeme bila kuwapa taarifa wateja wao na kusababisha uharibifu mkubwa wa vifaa vya majumbani, lakini pia na miundombinu ya viwandani. Je, Serikali sasa iko tayari kuanza kuwalipa fidia wateja wao wanaoathirika na kukatika kwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kunti Majala kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukatikaji wa umeme ni wa aina mbili, kuna kukata kwa vile tumepanga kukata ili tufanye matengenezo, lakini kukatika kwa sababu ya hitilafu ambazo ziko hata nje ya uwezo wa binadamu. Katika vitu ambavyo Shirika letu la TANESCO limejitahidi sana kufanya ni kutoa taarifa ya makatizo ya umeme yale ambayo tumeyapanga. Kiukweli katika hilo Myonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Tumewaelekeza na wamejitahidi katika siku za hivi karibuni matengenezo ambayo yanafanyika tunahakikisha tunayaratibu na taarifa zinatolewa kwa wateja wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye yale makatizo ambayo hatukuyatarajia, ni mashine imezidiwa kama ndugu zetu wa Kariakoo. Juzi tarehe 23 transformer moja ilipata hitilafu kwa sababu ilipokea mzigo mkubwa kuzidi ilivyotarajia, mvua zimenyesha, waya zimekatika na vitu kama hivyo. Tunaendelea kuhakikisha kwamba matukio hayo hayatokei. Hata hivyo tunaweza kufika kwenye utaratibu wa kawaida kuona namna gani ambayo sheria inaweza ikachukuliwa ili sasa ambaye anastahili kupata haki fulani anaweza kuipata kwa mujibu wa sheria tulizonanzo.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Umeme Wilaya ya Hanang kwa kuwa kwa sasa kituo kinachotumika ni cha Babati na hivyo inaendelea kuleta changamoto kubwa kwa watumiaji wa umeme ndani ya Wilaya ya Hanang?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asia Halamga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ilifanya utafiti na kubaini maeneo yanayohitaji Vituo vya Kupoza Umeme na vimetengwa katika awamu tatu. Kuna wale ambao wana mahitaji makubwa sana tumewaweka kwenye group la kwanza; kuna wale ambao mahitaji yao kidogo yanaweza kuvumilika wako group la pili; na kuna wale amabo wananaweza wakasubiri mpaka baadaye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mradi ambao niliotangulia kuutaja wa Grid Imara ambao unakaribia jumla ya trilioni moja na bilioni 900 unatekelezwa kwa miaka minne. Kwa kuanzia tumepewa bilioni 500 na tutajenga Vituo vya Kupoza Umeme 15 katika mwaka huu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaenda kuangalia kama eneo la Hanang ni eneo mojawapo ambalo limeoneka lina uhitaji wa kituo cha kujengwa haraka namna hii au kitakuja baadaye kidogo. Hata hivyo, nitoe taarifa njema kwa Waheshimiwa Wabunge, mradi huu utakapokamilika 2025/2026, tunatarajia kila wilaya itakuwa ina Kituo cha Kupoza Umeme cha Gridi katika wilaya husika ili kuzuia waya kuitembea kwa muda mrefu na hivyo umeme kupotea.
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitoe masikitiko yangu makubwa, nimekuja mara nyingi hapa kwa mradi wa REA II ambao ni Vijiji 25, ukizingatia huu mradi ulikuwa ni mradi wa mwaka 2014 ndiyo ulianza, hivi vijiji 25 vilitelekezwa. Nilikuja hapa mwaka jana mwezi wa Februari Bunge, Naibu Waziri mwenyewe hapa alisema kwamba Mwezi April mradi utakuwa umeshakamilika. Nimekuja Bunge la Mwezi wa Sita akaniambia mwezi wa Tisa mradi utakuwa umeshakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekutana na Waziri mwenyewe amekuja kufanya ziara kule nyumbani Jimboni kwangu, amefanya mkutano na wananchi pale Tukuyu akawaambia mpaka Disemba mradi utakuwa umeshakamilika. Leo hii naambiwa hapa kwamba mradi huu umechanganywa na REA Namba III Awamu ya Pili na utaisha Disemba, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda Wizara haikuelewa vizuri swali langu. Huu ni mradi REA II ambao ni wa muda mrefu, nilikuwa naomba nipate majibu. Ni lini mradi wa REA II vijiji 25 utakamilika?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, REA III Awamu ya Pili nilikuwa na Vijiji 36, mpaka ninavyoongea hapa ni Vijiji Vitatu tu ndiyo vimeshawashiwa umeme, kuna Kijiji cha Mboyo Kata ya Isongole, Kijiji cha Ndwati na Kijiji cha Lienje Kata ya Ikuti na deadline ilikuwa ni Disemba mwaka 2022. Leo naambiwa hapa kwenye swali la msingi kwamba tunapeleka tena mpaka Disemba 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri ni lazima tuwe serious kwa sababu wananchi wetu wanatusikiliza, ahadi Serikali wanazotoa nasi tunawaambia, leo naambiwa 2023 ndiyo mradi utakamilika. Naomba nipate ufafanuzi wa Serikali, mambo gani yaliyopelekea kubadilisha deadline kutoka Disemba 2022 mpaka Disemba 2023?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Anton Albert Mwantona kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama swali lilivyoulizwa ilikuwa ni kwamba ni lini Vijiji vilivyobaki katika REA II vitakamilishwa. Kule mwanzo vilipochukuliwa hivi Vijiji 25 vilitakiwa vifanyike katika REA II lakini havikufanyika vilibaki. Kwa sababu maelekezo ya Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ni kwamba hii Awamu ya REA III mzunguko wa pili usiache kijiji hata kimoja bila kupelekewa Umeme. Kwa hiyo, Vijiji hivi 25 vimeunganishwa kwenye Mkataba wa REA III Round II ili navyo vifanyiwe kazi na vikamilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupanga ni kuchagua tutawaelekeza wenzetu wanaotekeleza mradi kwenye maeneo haya ili wahakikishe kwanza katika scope hii wanashughulika na vile Vijiji ambavyo ni vya muda mrefu halafu hivi ambavyo vilikuwa ni vya REA III Round II waje wavimalizie kwa kadri tunavyosogea mbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lingine ambalo ni la msingi ameuliza kuhusu kubadilika kwa muda wa kumaliza mkataba wa REA III Round II kutoka Disemba mwaka jana kwenda Disemba mwaka huu. Sababu kubwa ziko mbili, kwanza ni ile ambayo tulikwisha ieleza ya matatizo tuliyoyapata ya kuongezeka kwa bei na changamoto zilizotokana na UVIKO, tatizo jingine ni tatizo chanya ambalo ni kuongezeka kwa Kilometa Mbili kwa kila Kijiji katika mradi huu ambao unaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo kwa scope ile ya zamani ambayo ilitakiwa iishe Disemba, baada ya kuongeza zaidi ya nusu ya ile scope imekwenda sasa kufikia mpaka Disemba mwaka huu, tutahakikisha kwamba tutavutana na kukabana na Wakandarasi ili hizi kilometa mbili ambazo zinaongezeka kwenye Vijiji vyetu Disemba mwaka huu kazi yote iweze kukamilika katika maeneo yetu.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Arumeru Magharibi wananchi wanahitaji umeme kwa asilimia 100. Kuna Mkandarasi ambaye yupo kwenye Jimbo hilo ambaye amekuwa akisuasua kuwapa wananchi umeme, kuna maeneo kuna maeneo amechimba mashimo, hakuna nguzo kwa muda mrefu, kuna maeneo ameweka nguzo hakuna nyaya kwa muda mrefu, maeneo mengine hakuna umeme kabisa....

MWENYEKITI: Sasa uliza swali lako Mheshimiwa.


MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, Je, Serikali inawaambia nini wananchi wa Jimbo la Arumeru Magharibi ambao wamesubiri umeme wa REA kwa muda mrefu bila mafanikio?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lemburis Noah Saputi, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika maeneo ambayo tulichelewa kupata Mkandarasi eneo la Arumeru ni mojawapo, Mkandarasi tayari amepatikana na anaendelea na kazi, katika maeneo ambayo tunaangalia kwa macho ya Karibu Mkoa wa Arusha pia ni mmojawapo. Tunahakikisha kwamba katika muda ambao tumekubaliana nae wa kimkataba kazi yake ya kupeleka umeme kwenye maeneo hayo itakamilika. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge tunaomba atupe subira kidogo na utatuona sana katika Jimbo lake tukiendelea kuvutana na Mkandarasi kuhakikisha kwamba kazi inakamilika katika muda tuliokubaliana.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.

Kwa kuwa tatizo la usambazaji wa umeme kupitia Wakandarasi wa REA III mzunguko wa pili imekuwa tatizo kubwa katika Majimbo yetu. Je ,Wizara haioni umuhimu sasa wa kutusikiliza Kikanda kuona matatizo yalivyo kwenye Majimbo yetu katika mradi huu wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swalil la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto zilikuwa nyingi, zile za ndani ya uwezo na nje ya uwezo. Changamoto zilizo ndani ya uwezo zote tumeshazitatua. Siku chache zilizopita Mheshimiwa Waziri aliitisha kikao cha Wakandarasi wote na kutoa maelekezo, tayari wenzetu wa REA wameshapita kwenye Mikoa takribani Saba au Nane ambayo tuliona iko nyuma zaidi kuhakikisha kwamba wao, watu wa REA na watu wa TANESCO kwa kushirikiana na Waheshimiwa Wakuu wa Mikoa lakini na Waheshimiwa Wabunge pia mlipata mialiko kwenye hayo maeneo tukae kwa pamoja ili tuone tatizo liko wapi na tuweze kusukuma shughuli hii ili tuweze kuikamilisha kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumewekeana makubaliano na tunaamini ndani ya muda tutayatekeleza na tutakamilisha kazi hizo.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona REA wanayo miradi mbalimbali lakini tunaotoka Majimbo ya Mjini na tunayo mazingira ya maeneo ambayo yana sifa za vijiji ingawa yako Mjini. Je, ni lini mtatupelekea umeme kwa sababu hata miradi hakuna huko, tunaona tu ya REA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Iringa Manispaa mtaa wa Ugele, Mtaragara, Msisina, Kagrielo na Wahe, ni lini mtatuletea umeme maeneo ya pembeni?(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jesca Msambatavangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wenye Majimbo ya Vijijini wamekuwa na miradi ya REA na densification na mingine, sisi ambao tuko kwenye Majimbo ya Mjini na mimi nikiwemo Jimbo la Bukoba Mjini, tumepata mradi unaoitwa peri-urban ambao kama nilivyotangulia kujibu kwenye siku zilizopita, mradi huu sasa umeenda kwenye awamu ya pili na tutakwenda kwenye awamu nyingine zinazokuja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilianza Mkoa wa Pwani na Kigamboni, awamu ya pili ikaja Mkoa wa Arusha, Dodoma na Mwanza, Awamu ya tatu imepata Mikoa mingine kama mitano au sita, sasa tutaenda awamu ya nne nimhakikishie Mheshimiwa Msambatavangu kwamba na Iringa pia itaingia kwenye awamu inayokuja kwa sababu pesa inapatikana taratibu lakini kila mmoja lazima apate pesa katika kufanya miradi hii kwenye maeneo yake.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Awali matarajio ya Serikali ilikuwa ni kuhakikisha maeneo haya ya vijiji vinawaka umeme ilipofika mwezi wa 12 mwaka jana, mwaka 2022, na ambapo ndio muda wa mkandarasi kukaa site ulikuwa unakamilika. Hata hivyo, mpaka ninapoongea hivi sasa, hivi vijiji maeneo mengi mashimo yamechimbwa na nguzo zimelazwa chini bado hazijasimamishwa.

Je, naomba kujua kauli ya Serikali; ni lini, hivi vijiji vitawashwa umeme kwa kuwa na muda wa mkataba wa mkandarasi umeshakwisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nicholaus Ngassa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuna mikataba iliyotakiwa kuisha Disemba mwaka jana. Hata hivyo, kama tunavyofahamu, tulipata changamoto ya kuongezeka kwa gharama za vifaa kipindi ambacho kulikuwa na magonjwa ya UVIKO. Pamoja na hayo tumepata faida nyingine ya kupata ongezeko la kilometa mbili kwa kila kijiji ambacho kilitakiwa kupelekewa umeme. Kwa hiyo vijiji vilivyo vingi upelekaji wa umeme utakamilika kufikia mwezi Disemba mwaka huu 2023. Kama nilivyosema kwenye majibu ya msingi kwenye baadhi ya maeneo kwa Mheshimiwa Ngassa, mwezi Aprili mwaka huu kuna maeneo ambayo tayari yatakuwa yamefikiwa na umeme kwa kadri alivyoiliza.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi. Naomba kuiuliza Serikali;

Je, ni lini vijiji 63 vilivyopo katika Jimbo la Newala Vijijini ambavyo havijawahi kuona umeme kabisa vitapatiwa umeme ili nao wawe wanufaika wa nishati hii muhimu? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Maimuna Mtanda, Mbunge wa Newala Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mhehsimiwa Mwenyekiti, wakandarasi katika Mkoa wa Mtwara na Lindi wako kazini wananendelea. Tumehimizana na wakandarasi walio katika maeneo hayo na kufatiliana nao kwa wakati ili kuhakikisha kazi yao inakamilika. Kama nilivyosema, ile kazi ya nyongeza na ya awali itakamilika mwezi Disemba mwaka huu 2023.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi. Ukosefu wa copper wire na mita ni moja ya sababu inayochelewesha uunganishwaji wa umeme katika Jimbo la Muhambwe, ikiwemo kata ya Busagara, Kitahara, Kumsenga na Mlungu;

Je, ni lini Serikali italeta vifaa hivi, ili kata hizi ziweze kunufaika na kuunganishiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Florence Samizi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa uzalishaji wa vifaa ulitokea katika maeneo mengi baadaya kupata matatizo ya UVIKO, na hivyo milango ilivyofunguliwa order zilikuwa nyingi na wahitaji walikuwa wengi, Kwa hiyo na sisi tunahakikisha tunatoa order za kutosha na kwa kadri zinavyozaliswha tunazipata. Nimuhakikishie tu Mheshimiwa Samizi kwamba, katika eneo lake na maeneo mengine vifaa vitapatikana na huduma kwa wananchi itaendelea kuunganishwa kwa sababu pesa tunayo na tunaendelea kufatilia kwa ajili ya upatikanaji wake.
MHE. ANNA R. LUPEMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Hiki Kijiji cha Kanoge hata kwenye ramani ya REA hakipo, pamoja na vitongoji vyake. Sasa ninaomba uhakika kwa sababu nimetokea huko hata kwenye ramani ya REA, ina maana kijiji hiki ni kijiji cha siku nyingi, kilirukwa sasa naomba commitment ya Wizara. Ni lini kitawekwa kwenye ramani pamoja na vitongoji vyake na wataingia katika mchakato wa kuwekewa umeme?

Mheshimiwa mwenyekiti, la pili, katika Kijiji cha Usense Kata ya Ulwira pamoja na Kijiji cha Nyamasi, Kata ya Ugala mpaka leo miti inaoza hasa naomba commitment ya Wizara;

Je, ni lini vijiji hivyo vitapata umeme, kwa sababu hakuna dalili kabisa ya kupatiwa umeme? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Lupembe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili nimuhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, kabla ya mwaka huu kuisha, vijiji hivyo alivyovitaja ambavyo vinaonekana havijafikiwa na huduma ya umeme, vitakuwa vimefikiwa kwa sababu kwenye mkataba wetu tumekubaliana kabla ya Desemba mwaka huu vijiji hivyo viwe vimepata umeme na zile changamoto tulizokuwa nazo tayari tumezitatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza naomba nikitoka hapa nitawasiliana nae kwa sababu sisi taarifa tulizo nazo kutoka site ni hizi. Kwa hiyo tutakaa pamoja ili tuweze kuziweka pamoja. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge wote kwamba baada ya mradi wa REA-3 awamu ya pili kupita hatutarajii kuwepo na kijiji chochote ambacho hakina umeme; na hayo ndio maelekezo ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Kwa hiyo tutahakikisha rekodi zetu zinakaa sawa ili kila kijiji kiweze kuwa kimepata umeme kwa kadri ya mkataba na maelekezo yaliyopo.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize swali dogo la nyongeza. Kijiji kidogo cha Msukanzi katika kata ya IIlula kimerukwa kuwekewa umeme lakini kata inayofuata kuna umeme. Sasa ni lini Serikali itaona umuhimu kwamba kuruka hivi vijiji si kitu kizuri, ili vijiji vyote viwe vinapata umeme kuliko kuacha kimoja hafu vingine vinapata?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum, Iringa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuhakikishie yeye pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote kwamba katika awamu hii ya tatu mzunguko wa pili ambayo ni ya mwisho hakuna kijiji kitakachoachwa. Tulipita humu Bungeni kwa Waheshimiwa Wabunge kuwaomba watuambie vijiji ambavyo vinadhani vimeachwa na tukavichukua tukaviweka kwenye orodha. Kwa hiyo kama kuna Mheshimiwa Mbunge yoyote anayedhani kuna kijiji ambacho kimerukwa kwa taarifa alizokuwa nazo basi tuwasiliane tukichukue kwa sababu sisi kwa taarifa tulivichukua vyote. Hata hivyo nitaenda pia kuwasiliana na Mheshimiwa Ritta Kabati, ili tukione hicho kijiji ambacho kimebaki tukichukue kama anavyosema.
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Ahsante kwa majibu mazuri. Pamoja na hayo nitakuwa na maswali mawili ya nyongeza. Lakini pia nitumie fursa hii pia kumshukuru Waziri wa Nishati, kulikuwa na mradi uliosimama wa Solar pale katika kijiji cha Kilambo na sasa amenihakikishia unatekelezwa na naona unaendelea. Namshukuru kwa hiyo hatua maana nchi itapata umeme lakini pia wananchi wangu watapata ajira.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilitoa tamko kwamba ifikapo 2022 Disemba tutakuwa tumemaliza changamoto za umeme kwenye vijiji. Katika Jimbo la Kalenga tuna vijiji vitatu ambavyo havina umeme vya Lwato, Makombe pamoja na Chamgo. Ni nini tamko la Serikali kutimiza hii ahadi yake?

Mheshimiwa Spika, swali la pili Serikali ilitamka kwamba itapeleka umeme kwenye vitongoji kwa maana ya umeme jazilizi, lakini tuna vitongoji vingi ambavyo vimekuwa na malalamiko kwa mfano kanisani pale Kiwele, Banawano pale Tosamaganga pamoja na pale Mangalali.

Je, ni lini Serikali itakamilisha suala hili? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kiswaga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali iliahidi kwamba itakamilisha umeme katika vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme kufikia Disemba, 2022 na ahadi hiyo bado ipo kwa sababu mikataba ilishasainiwa na wakandarasi wako site katika hatua mbalimbali za utekelezaji wa mradi huu wa REA wa 300 mzunguko wa pili na tunaamini kwa kuendelea kusimamia mikataba hii kwa wakati itakamilika ili vijiji vyote ambavyo vilikuwa havina umeme viweze kupata umeme.

Mheshimiwa Spika, katika eneo la pili ni kweli kwamba tunavyo vitongoji vingi ambavyo bado havijafikiwa na huduma ya umeme, lakini Serikali kama ilivyoeleza kwenye swali la msingi ni kwamba tayari umeme jazilizi utaanza kutekelezwa katika mwaka wa fedha ujao na kwa kadri ya pesa inavyopatikana huduma hii itazidi kuendelezwa kuhakikisha kwamba vitongoji vyote vinapata umeme na watumiaji wote wanaweza kupata umeme kwa wakati.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nikushukuru sana.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Ushetu lina changamoto kubwa sana ya umeme, hasa maeneo ya vijijini, maeneo ya shuleni, hospitalini na hata maeneo ambapo umeme upo unakatika katika sana.

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa uhakika kwa wananchi wa Jimbo la Ushetu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cherehani kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika bajeti ya Mwaka wa Fedha 2022/2023 Serikali imetenga takribani Shilingi Bilioni 400 ili kuboresha na kuimarisha gridi yetu ya Taifa na hivyo tunaamini baada ya kupata hizo pesa na mradi wa kuboresha gridi ya Taifa kutekelezwa, tatizo la kukatika katika kwa umeme litaendelea kupungua kwa sehemu kubwa.

Mheshimiwa Spika, pia katika eneo hilo umeme vijijini bado unaendelea kupelekwa kwa mikataba ambayo ipo na eneo la Shinyanga kwenye Jimbo lake ni eneo ambalo tayari lina Mkandarasi na anaendelea na kazi.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi. Maeneo mengi nchini wananchi wamehamasika kuomba umeme kwenye vitongoji vyao na vijiji. Katika Jimbo la Lupembe wananchi wangu wa Upami, Iyembela na maeneo mengine wamejaza fomu za kulipia umeme lakini kwa muda mrefu hawapewi.

Je, ni nini maelekezo ya Serikali inapotokea wananchi wamelipia umeme lakini hawaingiziwi kwenye maeneo yao?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Swalle wa Jimbo la Lupembe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna kipindi ambapo mahitaji ya umeme yalikuwa makubwa sana kwa sababu ya mazingira tuliyokuwa nayo kuliko uwezo wa TANESCO wa kuunganisha kwa wakati. Tunaendelea kujipanga na Serikali imeelekeza inapoanza Julai hatutarajii na hatutakiwi kuwa na kiporo cha zaidi ya mwezi mmoja nyuma, ndiyo mpango wa Serikali na imeongeza bajeti katika maeneo ya uunganishaji ili kuhakikisha kwamba basi mtu anapoomba umeme angalau ndani ya mwezi mmoja awe ameupata kuhakikisha kwamba anaweza kuutumia kwa wakati kwa mahitaji yake. (Makofi)
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mradi wa umeme wa Rusumo uliopo Wilaya ya Ngara ulitarajia kukamilika Desemba mwaka jana 2021 lakini mradi huo mpaka sasa haujakamilika.

Je, ni lini Serikali itakamilisha mradi huo ili kutatua tatizo la umeme Wilaya ya Ngara na Kagera kwa ujumla? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Oliver Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli mradi wa umeme wa Rusumo unaotarajiwa kuzalisha megawatts 87 unatekelezwa na ubia wa nchi tatu ambazo ni Tanzania, Ruanda na Burundi. Ni kweli ulitarajiwa ukamilike Desemba mwaka jana lakini kwa sababu ya changamoto za ugonjwa wa UVIKO-19 ambao wenzetu uliwakabili zaidi yetu, mradi huo umechelewa lakini maelekezo ya Serikali hizi tatu ni kwamba ifikapo Novemba mwaka huu mradi huu uweze kukamilika ili wale wananchi ambao Mheshimiwa Oliver anawafuatilia wa Jimbo la Ngara lakini na wa Mkoa wa Kagera kwa ujumla na Tanzania kwa ujumla waweze kunufaika na upatikanaji wa umeme unaotoka kwenye mradi huu wa Rusumo. (Makofi)
MHE. CONCHESTA L. RWAMLAZA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, transformer zinapoharibika na hasa vijijini huchukua muda mrefu bila kurejeshwa au kufanyiwa matengenezo na wakati mwingine inapita hata miezi sita.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba hizi transforme zinapoharibika zinarejeshwa kwa wakati ambao haumizi wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Conchesta Rwamlaza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli siku za nyuma manunuzi yalikuwa yanafanyika centrally na hivyo procedure zilikuwa zinachelewa kutoka kwenye Wilaya, Mikoa, Kanda mpaka kuja Taifa lakini kwa sasa TANESCO imeboresha utaratibu wake na kushusha manunuzi haya kwenye ngazi za Kanda mpaka kwenye ngazi za Mikoa na hivyo kurahisisha manunuzi kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwenye bajeti inayokuja ambayo tutakuja kuiwasilisha hapa imetengwa fungu la ziada la kufanya matengenezo kwenye maeneo haya, kwa hiyo pesa itapatikana kwa haraka na kuweza kurekibisha maeneo ambayo yatakuwa yanapata matatizo ili kuwapa huduma wananchi.
MHE. SYLVIA F. SIGULA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa na tatizo sugu la kukatika katika kwa umeme Mkoani Kigoma hasa katika Wilaya ya Kigoma Mjini na Kigoma Vijijini, mara zote umeme unakatika bila hata taarifa na kusababisha hasara kwa wananchi.

Je, ni nini maelekezo ya Serikali katika kutatua changamoto hiyo ili kupunguza hasara kwa wananchi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sylvia Sigula, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kigoma ni mmojawapo ya Mikoa ambayo haijafikiwa na gridi ya Taifa, lakini ziko njia tatu zinazopeleka umeme wa gridi ya Taifa katika Mkoa wa Kigoma na mojawapo ilielekezwa na Kiongozi wa Kitaifa Mheshimiwa Makamu wa Rais, kwamba ifikapo Oktoba mwaka huu iwe imekamilika ambayo ni ya kutoka Tabora kupita Uhuru - Nguluka kwenda mpaka Kidahwe.

Mheshimiwa Spika, kazi hiyo inaendelea kufanyika na tunataratijia kabla mwaka huu haujaisha kazi hiyo itakuwa imeisha, tunatarajia itaweza kuweka mazingira mazuri ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wetu wa Kigoma badala ya kutumia zile mashine za mafuta ambazo ziko kwa sasa na zinashindwa kuzalisha umeme wa kutosha kwa wananchi wetu wa Kigoma na hivyo mambo yatakuwa mazuri kabisa.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Pamoja na majibu haya marefu ya Serikali na historia ambayo hapa haitusaidii sana, dhamira ya Serikali pamoja na kujenga Bwawa la Mwalimu Nyerere pamoja na kuweka mahela kwenye mafuta ya petroli ambao watumiaji wa petroli wala hawahusiki na umeme huu vijijini.

Je, ni lini sasa Serikali itaangalia namna iliyo bora ya kupatana na wananchi ambao wanahitaji kuweka umeme kama wanashindwa kupunguza bei ili wapatane naye basi alipe sehemu ya gharama na gharama nyingine azilipe polepole kulingana na makubaliano watakayokubaliana, Serikali iko tayari kufanya jambo hili?

Mheshimiwa Spika, pili, kulikuwa na bei wakati huo Mheshimiwa hapa amejibu amesema ilikuwa shilingi 177,000 na shilingi 27,000 huko vijijini kabisa, vijiji miji ambayo kama Itigi ambao wameiondoa sasa katika ile laki moja na sabini saba kuja laki tatu ishirini. Je, Serikali iko tayari kurudisha vile vijiji miji ambavyo kutokana tu kupimwa eti tayari ni mji! Je, wako tayari sasa kuturejeshea katika ile bei ya shilingi 177,000?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahaya Massare, Mbunge wa Manyoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kulipa gharama za kuunganishwa umeme awamu kwa awamu au taratibu, tumeshaanza kuufanyia mkakati na majadiliano yanaendelea kuona namna bora ya kuweza kufikia azma hiyo. Changamoto kubwa ni kwamba gharama za bidhaa zinabadilika mara kwa mara, kwa hiyo mtu akilipa kidogo kidogo kwa muda ambao tutakuwa tumekubaliana, akamalize ndani ya muda huo labda pengine itatusaidia, lakini akichukuwa muda mrefu na pengine kushindwa kumaliza ndani ya ule muda tuliokubaliana, tutajikuta huduma hii inakuwa ni changamoto kwa kuitekeleza.

Mheshimiwa Spika, tayari wataalam wetu wa TANESCO wanaendelea kuangalia namna bora ya kuweza kupunguza hizi gharama za kuunganisha umeme kwa awamu moja kwa wateja wetu ili kuweza kufika azma ya kuwaunganishia wananchi wote umeme, lakini hasa kwenye maeneo ya mijini kwa sababu gharama za vijiji tayari zimepunguzwa.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, wenzetu wa TANESCO walishirikiana na wenzetu wa TAMISEMI kubaini na maeneo gani ya miji na ni maeneo gani ya vijiji na gharama ya vijijini ikabaki kuwa shilingi 27,000 na gharama za mijini zikasemwa hizi gharama nyingine ambazo tayari Serikali imeweka ruzuku ndani yake. Hata hivyo, Serikali ya Awamu ya Sita ni sikivu kwa wananchi itaendelea kufanya kazi kuendelea kuona namna ambayo inaweza ikawafikishia huduma bora Watanzania hata kwa kufanya majadiliano mengine ya kuona maeneo gani ipeleke kwa gharama gani kwa ajili ya kufikisha azma ya wananchi wote kupata umeme.

WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nampongeza Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri na napenda niongezee kidogo kwamba ni dhahiri kwamba yapo maeneo ya miji, kwanza tafsiri yetu ya miji na vijiji inatokana na sheria ya TAMISEMI, lakini dhahiri kwamba yako maeneo ya miji na majiji manispaa ambayo yako pembezoni yana sifa zote za maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa bahati nzuri tumebaini maeneo hayo na tumekubaliana na maombi ya Waheshimiwa Wabunge wengi pamoja na kwamba maeneo hayo yapo kwenye mipaka na miji na majiji lakini ukienda ukiona ni dhahiri kabisa kwamba yana sifa za maeneo ya vijiji kwa maana ya mazingira na hali ya kipato.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo katika bajeti ya Wizara ya Nishati tutatoa maelezo na utaratibu wa kuzingatia uhalisia wa maeneo haya katika kupanga bei ya kuunganisha. Ahsante. (Makofi)
MHE. BERNADETA K. MUSHASHU: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri ninayo maswali mawili ya nyongeza. Hadi sasa maeneo mengi katika Mkoa wa Kagera ambayo yamesambaziwa umeme wa REA umeme umefika tu kwenye ngazi ya vijiji haukuteremka chini. Swali la kwanza, je, ni lini sasa madi wa ujazilizi densification itaweza kuanza Mkoani Kagera ili vijiji vyote sasa na maeneo yote yaliyorukwa na vitongoji yaweze kupatiwa umeme?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; katika Mkoa wa Kagera kwenye Manispaa ya Bukoba tunazo Kata kama Kahororo, Buhembe, Nshambya, Nyanga, Kagondo, Kibeta, Kitendaguro na Ijuganyondo ambavyo pamoja na kwamba kata hizo ziko kwenye Manispaa ya Bukoba lakini zimekaa kama vijiji. Je, ni lini sasa Serikali itaanzisha mradi wa Peri- Urban ili sasa vijiji hivi au mitaa hii inayofanana na vijiji iweze kupata umeme wa REA kwa bei nafuu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bernadeta Kasasabago Mushashu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kwenye awamu ya kwanza upelekaji wa umeme vijijini tumefika hasa kwenye centres za yale maeneo na ni kwa sababu ya fedha iliyokuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, REA III round II peke yake ina shilingi trilioni moja na bilioni mia mbili na hamsini kwa ajili ya kufikisha umeme kwenye vile vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme. Azma na nia ya Serikali ni kuhakikisha kila mtu anapata umeme kwenye eneo lake na tayari nia hiyo imeanza. Tayari uko mradi wa ujazilizi tunaita Densification One ambao unaendelea katika baadhi ya maeneo yetu, lakini tumemaliza tayari upembuzi na kupata wakandarasi, tunaamini kufikia Julai densification 2(b) itaanza, lakini kufikia kwenye Oktoba densification 2(c) itaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado hii haitaweza kumaliza kwa sababu katika hizi densification tuna vitongoji karibu 5,000 na zaidi kidogo. Mnakumbuka hapa tayari Bungeni Mheshimiwa Waziri amesema kwamba tunatafuta mkakati mkubwa wa kuweza kupata fedha nyingi karibia trilioni sita kwa ajili ya kupeleka sasa umeme kwenye vitongoji vyote vilivyobaki nchini ambavyo havina umeme. Kwa hiyo kadri pesa inavyopatikana vitongoji vitazidi kupelekewa umeme kwa kadri Serikali inavyozidi kujipanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili la Peri- Urban, nimshukuru Mheshimiwa Bernadetha kwa kuulizia kuhusu Jimbo la Bukoba Mjini, makofi yalikuwa mengi, swali sikulisikia vizuri, lakini naamini alichokizungumzia ni peri-urban na tayari Serikali imeshatangaza na imefikia hatua za mwisho za kupata wakandarasi wa kupeleka umeme katika maeneo ya mijini lakini yenye uso wa vijiji kama alivyozitaja hizo kata saba za Jimbo la Bukoba Mjini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mikoa mingine kama tisa katika awamu hii ya peri-urban nayo kufikia Julai tunaamini mradi huu utaanza kwa ajili ya kufikisha umeme katika maeneo haya kwa ajili ya kupata umeme kwa gharama nafuu.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa fursa hii ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba sasa Serikali inijibu, ni kwa nini mkandarasi wa REA Ngara amepotea site, haonekani kwa takribani kipindi cha miezi mitatu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ndaisaba, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, awamu ya upelekaji wa umeme vijijini iko na awamu tofautitofauti, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kuna upembuzi yakinifu, ku-survey yake maeneo, uagizaji wa vifaa na hatua ya mwisho ya uwekaji wa miundombinu yenyewe. Maeneo hayo na mazingira hayo ya hatua hizo yanaweza kufanya mkandarasi asionekane site kwa muda na hasa pale anapokuwa kwenye hatua ya kuagiza vifaa. Naamini maeneo mengi wengine vifaa vimefika, wengine bado, kwa hiyo sehemu ambapo hajafika, naamini itakuwa labda alichelewa kwenye kuagiza vifaa, lakini vifaa vitafika, kwa sababu maelekezo yetu ni kabla ya Desemba mwaka huu miradi iwe imekamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kuwaelekeza wakandarasi wote kuendelea na kazi katika site zao kulingana na schedule walizoziweka na vifaa vilivyopo ili tuweze kufikia deadline ya Desemba kuweza kufikisha umeme kwenye maeneo hayo.
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kata ya Mbaramo na Shagayo katika Jimbo la Mlalo bado hakuna hata kijiji kimoja kimesambaziwa umeme. Nataka kujua, ni lini Serikali itaanza usambazaji wa umeme katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shangazi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Tanga unao wakandarasi watatu wanaopeleka umeme vijijini na katika Jimbo lake yuko Mkandarasi anaitwa Dem Electric ambaye anapeleka umeme katika maeneo hayo. Nafahamu kwamba mkandarasi huyu anajitahidi kufanya kazi zake vizuri na atakuwepo kwenye maeneo ya kazi, pengine ameanzia eneo lingine ili aje amalizie kwenye hayo maeneo ya kata alizozisema za Mbaramo na Shagayo kama nitakuwa nimezitaja vizuri. Nichukue nafasi hii kumwelekeza yeye pamoja na wakandarasi wengine wagawanye magenge wanayotumia katika kufanya kazi ili kila eneo la Mbunge liweze kuonekana likiwa linafanyiwa kazi kama ambavyo walienda wakaripoti wakaanza kufanya kazi za utekelezaji katika maeneo hayo na eneo hilo liwe mojawapo la kuhakikisha kwamba wanatoka kwenye maeneo waliyofikia sasa kwenda kwenye maeneo mengine ili kufanya kazi na kukamilisha kazi kwa wakati.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa Jimbo la Hai kuna changamoto kubwa sana ya uchakavu wa miundombinu, lakini kumekuwa na maombi ya muda mrefu sana ya wananchi tangia mwaka 2008 mpaka sasa hivi hawajaunganishiwa; na kwa kuwa tulikaa na Mheshimiwa Waziri na timu yake na wakapeleka wataalam kule Hai kwenda kubaini mahitaji ya wananchi. Je, ni lini Serikali itatuletea vifaa ili wananchi waweze kuunganishiwa umeme na kurekebisha miundombinu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Mheshimiwa Saashisha amefuatilia sana umeme katika jimbo lake na kama alivyosema Mheshimiwa Waziri alituma timu kwenda kufuatilia. Niombe kwamba baada ya hapa tukutane ili nipate taarifa ya hiyo Kamati na nitoe maelekezo ya kufanya kile ambacho kilibainika kinaweza kufanyika ili tatizo lake la muda mrefu ambalo amekuwa ukilifuatilia liweze kutatuliwa. Naomba baada ya hapa tuweze kuwasiliana.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, niishukuru na kuipongeze Serikali kwamba imeongeza kilometa mbili za usambazaji wa umeme katika kila kijiji na kuifanya kilometa tatu badala ya kilometa moja; je, ni lini sasa Serikali itaanza utekelezaji huo wa kujazilizia kilometa mbili ili kila kijiji kipate kilometa tatu za usambazaji wa umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Spika,swali la pili, kwa kuwa mradi huu wa REA vijijini ni mradi wa umeme vijijini; je, ni lini sasa Serikali itapeleka umeme vitongojini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kungu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza ni kweli Serikali ya Awamu ya Sita iliongeza kilometa mbili kwa kila kijiji ambacho kipo katika Mradi wa REA III Round Two ambao unaoendelea kutekelezwa. Kazi iliyofanyika ni kupitia maeneo yale ya vitongoji na kuyabaini ili hizo kilometa mbili zionekane wapi zipelekwe.

Mheshimiwa Spika, ninavyozungumza majadiliano na wakandarasi yanaendelea na tunaamini kuanzia mwanzoni mwa wiki inayokuja hiyo mikataba ya adendum mikataba ya nyongeza ya kupeleka umeme kwenye hizo kilometa mbili itasainiwa na hivyo tunatarajia mwanzoni mwa mwezi wa tano wakandarasi wataingia site kuendelea sasa na hiyo kazi ya kupeleka umeme katika hizo kilometa mbili za nyongeza ambazo zinatakiwa ziongezwe.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili kwamba ni lini umeme utapelekwa vitongojini. Nipende kusema hata sasa umeme unapelekwa kwenye vitongoji, Miradi ya rea inapeleka umeme vijijini ambapo vijiji vinaenda kwenye vitongoji, lakini upo mradi maalum wa densification 2B ambao unaendelea katika vijiji karibu 1,600 na wakandarasi tayari wameripoti site na wanapeleka umeme katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, lakini kubwa zaidi Serikali ipo katika taratibu za mwisho za kutafuta fedha kupeleka umeme kwenye vitongoji karibu 6101 ambavyo bado havijapata umeme na inahitajika takribani shililingi trilioni 6.5 ambayo tunaamini tutaipata kwa mbinu ambazo tayari tumepeleka maombi yetu Serikalini na mchakato wa kutafuta pesa hiyo unaendelea. Hivyo katika miaka minne mitano tunatarijia kuwa tumemaliza vitongoji vyote ambavyo havina umeme na huo ndio mpango wa Awamu ya Sita.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Spika, Je, ni lini Wizara itatekeleza maelekezo ya Mhesimiwa Waziri January Makamba kwa kurejesha bei ya kuunganisha umeme kwa Tarafa ya Ifakara mathalani maeneo yote yale ambayo yana asili ya vijiji 27000 kwa mfano Katinduka B na C.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utaratibu wa kubaini maeneo ya kupelekea umeme kwa gharama ndogo ulifanyika lakini haukuwa makini vya kutosha kwa hiyo tumewaelekeza wenzetu wa TANESCO warudie zoezi hilo tena kwa kuwa - consult Waheshimiwa Wabunge wote ili tupate maeneo hayo na kuyafanyia kazi sahihi.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha unaharakisha na kukamilisha kupelekwa kwa umeme kwenye vijiji vya Wilaya ya Korogwe kwa sababu mkandarasi wake anasuasua sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli mkandarasi anayepeleka umeme kwenye Wilaya ya Korogwe pamoja na nyingine mbili anazembea sana na tumekubaliana achukuliwe hatua na itakapofika katikati ya mwezi huu kama atakuwa hajafikia yale makubaliano tuliyofikia basi hatua stahiki zitachukuliwa ikiwemo pamoja na kuvunja mkataba wake ambao ameshindwa kuutekeleza kwa wakati.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona; je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya umeme wa REA katika Kijiji cha Tilawandu ambacho kilisahaulika katika awamu zilizopita za utekelezaji wa umeme wa REA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu naomba kujibu naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Francis Ndulane, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vijiji vyote ambavyo vilikuwa havina umeme vipo katika mradi wa REA Awamu ya III Mzunguko wa Pili na kwa sasa tuna takribani vijiji 2,600 tu ambavyo vimebaki havina umeme kabla ya Desemba vitakua vyote vimepata umeme.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mhesimiwa Spika, nashukuru, ni, lini Serikali itakamilisha usambazaji umeme kwenye visiwa vidogo vilivyoko nje ya Gridi ya Taifa Jimboni Ukerewe? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa ya Mheshimiwa Joseph Mkundi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tumeshatangaza zabuni tayari kwa ajili ya wapelekaji wa umeme katika maeneo ambayo hayajafikiwa na Gridi na kinachofanyika sasa ni mchakato wa kubaini bei na uhalisia wa huduma yao ili tuweze kufikisha umeme katika maeneo ambayo Gridi ya Taifa haijafika.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Vijiji 34 Mbogwe havijawekewa umeme kabisa, ni lini vitawekewa umeme, vijiji vya Mbogwe ambavyo havijapata umeme toka dunia iumbwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maganga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vijiji vyote ambavyo havina umeme viko katika mradi wa REA III Round Two na tunaendelea kusimamia na wakandarasi kuhakikisha kabla ya Disemba hii kukamilika basi vijiji vyote vimepata umeme kwa mujibu wa mikataba yetu.
MHE. ALLY A. J. JUMBE: Mheshimiwa Spika, ETBICO ni Kampuni ambayo inasambaza umeme Mkoani Mbeya, wanaenda vijijini, kwa mfano Kijiji cha Bukunelo, Kijiji cha Ikama wanasema wamewasha umeme na taarifa Serikalini ni kwamba imewasha umeme, wakati huo wamewasha transformer zinaunguruma na umeme wenyewe kwa wananchi haujafika, je hiyo ni sahihi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Ally Jumbe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuwasha umeme kwa mwananchi ni kumwashia katika nyumba yake na eneo lake analohitaji umeme. Kwa hiyo, kama wanasema wamewasha kwenye transformer hiyo sio sawa na tutalifuatilia kuhakikisha kwamba umeme unawafikia wananchi kwa sababu ndio wanaouhitaji. (Makofi)
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Kata ya Isakamariwa, Kilinginira, Kilungu, Mwamwashiga na Mtungulu mkandarasi kaweka nguzo, je, ni lini atakamilisha kuweka waya wawashe umeme? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali mawili la nyongeza la Mheshimiwa Ngassa, kwamba kabla ya Disemba hii kuisha vijiji vyote na kata zote na maeneo ambayo yapo katika Mradi wa REA III Round Two yatakuwa yamewashiwa umeme.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Spika, nashukuru, ni mara ya tatu au zaidi nauliza hili swali nilitaka kufahamu ni lini Mkoa wa Kagera utaunganishwa kwenye Gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tayari fidia imeshafanyika katika njia ya kutoka Benako kuja Kyaka kwa ajili ya kupitisha umeme utakaotoka Nyakanazi na Rusumo kuja katika Mkoa wa Kagera na Serikali kupitia BADEA imepata fedha za utekelezaji wa mradi huo, kwa hiyo, siku sio nyingi mambo yataanza kufanyika katika eneo la site.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napongeza Serikali kwa majibu mazuri juu ya hatua ya mwendelezo wa Mradi huu muhimu wa uzalishaji wa umeme wa jua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu ni moja tu la nyongeza, kwamba ni kwa namna gani zana ya ushirikishwaji wa jamii inayohusika na hasa juu ya masuala ya fidia, imekuwa ikizingatiwa lakini pia suala zima la uongozi hasa wa ngazi za chini Serikali za Mitaa umekuwa ukihusishwa hili kuona kwamba michakato ya haki na tathmini iliyo halali kwa ajili ya malipo kwa wananchi inazingatiwa? Naomba kujibiwa.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Butondo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimshukuru Mheshimiwa Butondo kwa kulifuatilia jambo hili mara kwa mara, lakini namhakikishia kwamba kama anavyofahamu na anavyoona limefikia mwisho na mambo yanakwenda vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye jibu la msingi nimesema malipo ya fidia yataanza kufanyika mwishoni mwa mwezi huu, lakini taratibu zote zote za fidia zimepitiwa kama ambavyo zinaelekezwa na sheria. Kwa hiyo wale wataoathirika wote tayari wamebainishwa na wameshirikishwa katika mchakato huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo jambo zuri sana ambalo naomba kulisema kwa sababu ya uhitaji mkubwa wa umeme tuliokuwanao tumekubaliana na wenzetu wa TANESCO na Serikali imewaagiza watoe pesa zao kwanza kuanza kulipa fidia haraka kama mkopo, halafu badae Wizara ya Fedha itakapokuwa imelipwa watarudishiwa kwenye eneo lao. Kwa hiyo wiki hii ambayo tumeianza jana wananchi kule wataanza kulipwa fidia katika mazingira yao ili kuhakikisha kwamba mradi hii unakimbizwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaelekeza wenzetu wa TANESCO watakapoenda kulipa fidia kupitia halmashauri, kupitia Serikali za Vijiji na Viongozi wetu wa Serikali waliokuwa nao washirikiane hili kuwabaini wale ambao ni waathirika halisi na waweze kupewa haki yao stahiki kwa mujibu wa sheria hili mradi uweze kutekelezwa bila tatizo lolote.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa kunipa nafasi. Mradi wa REA wa vijiji 26 Wilaya ya Tanganyika ambao Mheshimiwa Naibu Waziri, alikuja akauzindia mpaka sasa haujakamilika. Je, ni lini Serikali itakamilisha ule mradi ili uweze kuleta tija kwa wananchi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Selemani Kakoso, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli nilienda kuzindua Mradi huo mimi mwenyewe na Mkandarasi anayetekeleza Mradi huo Mkandarasi wa ITIBIKO bado anaendelea na kazi site na makubaliano tuliyokuwanayo ni kufikia Desemba mwaka huu mradi huu pamoja na miradi mingine yote ya kupeleka umeme vijijini iwe imekamilika. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Kakoso kwamba jambo hili tunalifuatilia na kabla ya mwaka huu kwisha tutahakikisha ya kwamba kazi hiyo inakamilika katika eneo lake la Wilaya ya Tanganyika lakini na maeneo mengine.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; Serikali sasa ina mpango gani wa kuendelea kujenga vituo hivyo vya kuuza gesi asilia katika mikoa ya mingi Tanzania hususani Mkoa wa Rukwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali sasa imejipangaje kupunguza bei ya vifaa vinavyotumika kurekebishia mfumo wa magari kwenye mafuta na kwenye kit ya kujazia gesi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bupe, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwenye jibu la msingi kama nilivyosema Serikali imejipanga vipi kuongeza Vituo vya Kujaza (CNG), tayari vibali kwa wakandarasi na wawekezaji 20 vimetolewa kwa ajili ya kwenda katika maeneo mbalimbali kuweza kuongeza wigo wa eneo hili. Tunaendelea kuvutia wawekezaji mbalimbali waje kuwekeza katika eneo hili la gesi asili ambalo litakuwa linatumika katika maeneo mbalimbali. Kwa hiyo michakato hiyo inaendelea na Serikali katika mwaka huu wa fedha itajenga hivyo vituo vyetu viwili ambao tunaamini kabla ya mwaka huu wa fedha kwisha vitaanza utekelezaji wake maeneo ya Mlimani City na maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, Serikali inafanya nini kuhakikisha bei ya hizi zinazoitwa conversion kits zinapungua. Mojawapo ya kitu tunachokifanya tunahamasisha watu wengi wanaoweza kuja katika biashara hii ya kutengeneza conversion kits waje, biashara ikisha kuwa na watu wengi wanaoshiriki automatically ushawishi utakuwa ni mkubwa na gharama tunatarajia zitapungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile pia tumewaza namna ambayo tunaweza tukashirikiana na wenzetu wa Wizara

nyingine za Kisekta, Wizara ya Fedha na wengine kuona namna ya kuweka fedha au punguzo la kodi kwenye vifaa hivi kwa watalam watakavyoshauri ili tuone namna ambavyo tunaweza tukapunguza gharama za hizi conversion kits ili kuweza kuvutia watu wengi zaidi kuweza kuingia katika eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo la mwisho, tayari vituo vinavyouza gesi vimeweka utaratibu wa kukopesha wale wanaokuwa na haya magari wanaotaka kufanya conversion kit wanawakopesha na wanakuwa wanalipa kidogo kidogo kwa sharti la kwenda kuchukua gesi katika kituo chake hizo zote ni mbinu katika kuhakikisha kwamba gharama zinapungua na watumiaji wanaweza kupatikana kwa wingi.
MHE. NANCY H. NYALUSI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Tunaishukuru Serikali kwa utekelezaji, hata hivyo, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; je, ni lini Serikali itakamilisha kupeleka umeme katika Kijiji cha Idunda na Funuti, Kata ya Kimara katika Wilaya ya Kilolo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, ni lini Serikali itaanza kusambaza umeme katika Vitongoji Mkoani Iringa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili nyongeza la Mheshimiwa Nancy Nyalusi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema katika jibu la msingi Vijiji vya Mufindi vitakamilika mwezi wa Sita mwaka huu kwa mujibu wa Mkataba, lakini vijiji vingine vyote nchini kama alivyovitaja yeye vya Kilolo kabla ya Desemba mwaka huu vitakuwa vimefikishiwa umeme kwa mujibu wa mkataba wetu tuliokuwa nao kwenye REA three, round two. Kwa hiyo nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Nyalusi pamoja na Waheshimiwa wengine, kwamba jambo hili tunalisimamia kwa karibu zaidi kuhakikisha kwamba umeme unafika katika Vijiji vyote kabla ya mwaka huu kuisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la pili, tunaendelea kutafuta pesa ambayo itatuwezesha kupeleka umeme katika vitongoji vyote karibu 36,000 tulivyokuwa navyo nchi nzima katika miaka minne, mitano inayokuja kwa gharama ya Sh.6,500,000,000,000. Taratibu za kutafuta fedha hizi zinaendelea na zitakapokuwa tayari, basi zitaletwa kwa umma hili kazi hii iweze kufanyika na kuhakikisha vitongoji vyote vinapata umeme. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mwezi Desemba Meneja Mkoa wa Iringa ndugu yangu Jumbe aliniahidi kupeleka umeme katika Kijiji cha Usengerenidete, mpaka sasa nimeshapelekwa kwenye vyombo vya habari mara nne, je, ni lini sasa TANESCO watatoa angalau fedha za dharura kutoka Makao Makuu watupelekee hili hao wananchi wapate umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Jackson Kiswaga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ameomba yeye mwenyewe fedha za dharura na jambo hili nilikuwa sijalipata naomba baada ya session hii ya maswali, niende kwake tukajadiliane, nijue tatizo ni nini na tuweze kulitatua tatizo hilo ili wananchi waendelee kupata huduma hiyo ya umeme. (Makofi)
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa fursa ya swali dogo la nyongeza. Mkandarasi anayetekeleza Mradi wa REA ndani ya Mkoa wa Rukwa speed yake ni ya kusuasua sana, hususani ndani ya Jimbo langu la Kwela kufikia mwezi Machi katika vijiji 54 alikuwa amewasha vijiji tisa. Nataka kujua comittment ya Serikali leo ili wana Rukwa na Jimbo la Kwera wajue nini hatima yao kupata umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Deus Sangu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe comittment ya Serikali kwamba ile mikataba yote ambayo ilitakiwa kwisha Desemba mwaka huu kwa wale wakandarasi ambao wanaendelea na kazi hizi, tutaendelea kuwasimamia kwa karibu zaidi. Tumeshawekeana deadline na timeline za mambo mbalimbali na wale ambao wanaendelea kuzikiuka taratibu ambazo tunazichukua za kisheria watazipata muda si mrefu. Kwa hiyo niwahakikishie kwamba watapata umeme kabla ya muda wa mkataba kwisha na wale ambao watashindwa tutachukua hatua mapema ili tuweze ku– rescue situations kupata wakandarasi wengine ambao watakamilisha upelekaji wa umeme katika miradi ambayo tumekubaliana.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa, zoezi la upelekaji umeme kwenye Miji na maeneo yanayofanana na Vijiji bado haijakamilika kama inavyotakiwa.

Je, ni lini, Serikali itahakikisha maeneo yote yaliyoko Mijini hasa kwenye Kata za Buhongwa, Runhima na Kishili yanapata umeme uliokusudiwa kwa wakati na wananchi waweze kufaidi matunda hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stanslaus Mabula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli zimekuwepo awamu mbili za kupeleka umeme kwenye maeneo ya Mijini yenye picha ya Vijiji ambayo tunaita miradi ya peri-urban, katika Jiji letu la Mwanza awamu ya kwanza ilifika ambayo iligusa pia, maeneo ya Dar es Salaam, Arusha na Mwanza. Ipo awamu ya pili ambayo ilikuja Dodoma na Mbeya na sasa iko awamu ya tatu ambayo kuna baadhi ya maeneo tayari imeshaanza kufanyika, Mkoa wa Kagera Jimbo la Bukoba Mjini likiwa ni mojawapo Geita, Mbeya tena Tanga na maeneo mengine ambayo yana uso wa Vijiji lakini yako Mjini yanaendelea kupelekewa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninamuahidi Mheshimiwa Mabula pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine ambao Majimbo yao yako Mjini kwamba miradi hii inaendelea kufanyika kadri ya upatikanaji wa fedha awamu kwa awamu. Pale ambapo tunapambana kuhakikisha kwamba REA III round II inakamiliishwa kwenye vijiji, vivyo hivyo ndivyo tunavyopambana kutafuta pesa kwa ajili ya kupeleka umeme katika maeneo ya Mijini lakini yenye uso wa Vijiji.
MHE. EMMANUEL P. CHEREHANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Serikali ina mkakati gani wa kuongeza Mkandarasi katika Wilaya ya Kahama yenye Halmashauri mbili Ushetu pamoja na Msalala kutokana na aliyepo kupeleka umeme kwa kusuasua sana?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cherehani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkandarasi anaepeleka umeme katika Wilaya ya Kahama ni Mkandarasi anayeitwa Tontan ambaye tunakiri ana mapungufu na hasa katika kazi yake anayoifanya Tanga na tumewekeana masharti ya kutimiza, akishindwa kuyatimiza mwezi huu wa Nne hautaisha ataondoka site zetu ili tuweze kupata Mkandarasi mwingine wa kupeleka umeme katika maeneo hayo. Kwa hiyo wananchi wa Kahama ninawaahidi kabisa kwamba umeme katika maeneo yao utapelekwa na utakamilika kwa wakati kwa sababu ni jambo linalotakiwa kukamilika kwa wakati.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali. Pamoja na Mkandarasi anayetekeleza kazi kwa Jimbo la Mbulu Vijijini kusuasua, sasa ameanza kuweka nguzo katika kila Kijiji, vingine nguzo 12, 13 na 15.

Je, ni kiasi gani cha nguzo kinatakiwa kiwekwe kila Kijiji ili sisi tusimamie?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, pesa iliyokuwa imepatikana katika awamu ya kwanza ya REA III round II ilikuwa unawezesha nguzo takribani 20 kupelekwa katika kila Kijiji, lakini tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, alisikia kilio cha Watanzania na akatafuta pesa ya ziada na kuongeza, kwa hiyo kila Kijiji kitapata takribani kilomea Tatu ambazo ni 20 mara Tatu maana yake karibia nguzo 60 katika awamu hiyo inayokuja ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninawaahidi Waheshimiwa Wabunge wote kwamba kutoka nguzo 20 sasa tutapata nguzo 60 katika kila Kijiji kwa ajili ya kuongeza wigo wa upelekaji wa umeme katika maeneo hayo. Tunakamilisha taratibu za kusaini mikataba kwa Wakandarasi ambao wanaonekana wanaweza wakaongezewa kazi katika maeneo yao ili waongezewe katika kilometa Mbili ambazo wanatakiwa kuzifanya katika vijiji vyote ambavyo tunavimalizia katika mradi huu wa mwisho wa REA III round II.
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali yanayotia moyo, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, la kwanza. Kilwa Kisiwani kwa sababu ni kisiwa utaratibu wake ni wa kipekee. Je, na yenyewe nayo imo katika mpango huu na awamu hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Kata za Nanjirinji, Narikalage pamoja na vijiji vyake vya Nainokwe, Liwiti pamoja na Narikilage yenyewe inapitiwa na msitu wa hifadhi na kulikuwa na mgogoro kati ya REA na TFS: Je, mgogoro huo umekwisha na Serikali sasa iko tayari kusambaza umeme katika kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikianza na swali la kwanza, tunafahamu kwamba kuna vijiji katika Jimbo la Kilwa Kusini ambavyo vipo katika visiwa na upo mradi unaitwa RBF (Result Based Financing) awamu ya pili ambao utafikisha umeme katika visiwa hivyo pamoja na visiwa vingine Tanzania Bara 36 katika awamu hii. Kwa hiyo, pamoja na visiwa hivyo viwili, viko visiwa vya maeneo mengine vya maeneo mengine ambavyo pia vitafikishiwa umeme katika miradi hii ambapo tunatafuta sasa wakandarasi wa kupeleka mradi wa umeme katika maeneo hayo. Kwa upane wa Kilwa amepatikana Mkandarasi anaitwa Greenl Leaf ambaye anakamilisha taratibu za kupeleka umeme katika maeneo hayo ya visiwa.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili, ni kweli tulikuwa na changamoto ya mawasiliano katika ya Wizara ya Nishati na Wizara ya Maliasili na Utalii kupitisha miundombinu ya umeme katika mapori ya TFS, lakini tatizo hilo sasa limekuwa solved, na sasa tunazungumza lugha moja. Kwa hiyo, sasa kunapokuwa na mradi unaohitaji kupita katika maeneo hayo, vibali vinatolewa na mradi unaweza kupitishwa kwa wakati.

Kwa hiyo, kwa sasa tatizo hilo limetafutiwa ufumbuzi na halina tatizo.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Pamoja na utekelezaji wa REA III unaoendelea Wilaya ya Nkasi lakini umeme unakatika kupita kawaida: Serikali ina mpango gani wa haraka wa kutatua changamoto hii ambayo wananchi wangu wanapata hasara kubwa hasa wanaosindika Samaki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, wenzetu wa Nkasi wanapata umeme kutoka nje ya nchi, lakini mradi wa Gridi Imara unapeleka Gridi ya Taifa katika Mkoa wa Katavi ambao utafika pia katika Mkoa wa Rukwa na maeneo hayo. Kwa hiyo, ndani ya miezi kama 18 tatizo hili litakwisha kwa sababu tutakuwa tumefikisha umeme wa gridi kwenye maeneo hayo ambao ni umeme wa uhakika na ambao tunaweza tukau- control sisi wenyewe katika maeneo hayo.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je, ni lini sasa mtaweza kufunga transformer mliyokuwa mmeahidi tangu Desemba ili kupunguza adha ya kukatikatika umeme kwenye Jimbo la Temeke? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dorothy Kilave, Mbunge wa Temeke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, transformer iliyotakiwa kuwekwa katika eneo la Temeke ipo katika mchakato wa manunuzi kwa sababu tayari pesa ilishatengwa na uamuzi ulishafanyika, hivyo katika miezi miwili au mitatu inayokuja tunaamini taratibu za manunuzi zitakuwa zimekamilika na transformer itafungwa kwa ajili ya kuongeza uwezo wa umeme katika maeneo hayo kuweza kuwahudumia wananchi wote.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Ni lini Serikali itapeleka umeme katika vitongoji 192 katika Wilaya ya Buhigwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kavejuru, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa REA III Round II ambao unaendelea kutekelezwa katika maeneo mbalimbali tuliyokuwa nayo unaendelea kupeleka umeme katika vitongoji mbalimbali ambavyo vimo ndani ya vijiji. Pia, upo mradi wetu wa densification (ujazilizi awamu ya pili) ambao pia unaendelea kupeleka umeme kidogo kidogo katika maeneo ya baadhi ya vitongoji. Kwa awamu hii tuna vitongoji kama 2,630.

Mheshimiwa Spika, ili kumaliza tatizo hili la umeme katika vitongoji, Serikali ipo katika taratibu za kutafuta fedha takribani shilingi 6,500,000,000,000 kuhakikisha kwamba inapeleka umeme kwa mkupuo mmoja katika vitongoji vyote, takribani kama 36,000 tulivyokunavyo Tanzania Bara ambavyo havijafikiwa na umeme. Tunaamini mradi huu utakamilika na katika miaka mitatu au minne au mitano ijayo vitongoji vyote vitakuwa vimepata umeme.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mafinga tunaishukuru Serikali kwa kutufikishia umeme katika kila kijiji, hata hivyo vitongoji vingi havina umeme: Je, ni lini vitongoji vitaanza kupata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Cosato Chumi, Mbunge wa Mafinga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema katika swali lililotangulia la Mheshimiwa Kavejuru, Serikali ipo katika mpango mkakati mkubwa sana wa kutafuta fedha kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote takribani 36,000 ambavyo vimebaki Tanzania Bara ambavyo havijapatiwa umeme kwa mradi utakaogharimu karibia Shilingi 6,500,000,000,000/=. Kwa hiyo, taratibu zitakapokamilika kila eneo linalohitaji umeme litafikishiwa miundombinu ya umeme katika vitongoji vyetu.
MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Naibu Waziri matatizo ya mkandarasi wa REA aliyepewa tender ya kusambaza umeme kwenye Mkoa wa Songwe unayafahamu. Mpaka sasa hivi katika ya vijiji 127 amepeleka umeme kwenye vijiji 48 tu: Sasa hamwoni wakati umefika wa kuvunja naye mkataba kunusuru Mkoa wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa George Mwenisongole, Mbunge wa Songwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna baadhi ya maeneo ambapo Wakandarasi wetu hawajafanya vizuri. Tunachokifanya kikubwa ni kuhakikisha tunawasimamia kwa karibu kuhakikisha kwamba kazi zao zinakamilika kwa wakati. Katika eneo la Songwe, tumekuwa tukilifuatilia kwa karibu na Mheshimiwa Mwenisongole na tunamhakikishia kwamba ndani ya muda stahiki mradi huo utakamilika.

Mheshimiwa Spika, katika wale Wakandarasi ambao wako nyuma sana na hatuna namna, tutavunja mikataba yao, lakini wale ambao wanaweza kufanya kazi na kuikamilisha kwa wakati, tutasimamia vizuri ili tuweze kuikamilisha kwa wakati kwa sababu kuvunja mkataba pia siyo option nzuri ya kukamilisha mradi kwa wakati.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Serikali ilituahidi kutuletea mkandarasi kwa ajili ya kukamilisha vitongoji 47 vilivyoko ndani ya Jimbo la Hai: Ni lini mkandarasi huyo ataanza kazi ya kukamilisha kwenye vitongoji hivi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Saashisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli taratibu za kumpata mkandarasi wa kwenda kukamilisha umeme katika maeneo ya Hai na maeneo mengine ya Kilimanjaro ambayo yalikuwa yameshamaliza level ya vijiji yanaendelea na tunaamini katika miezi miwili ijayo Mkandarasi atakuwa amepatikana, na ataenda kuingia site sasa kuweza kupeleka umeme katika maeneo hayo ambayo yalikuwa hayajafikiwa na umeme.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi niulize swali la nyongeza. Vijiji vingi katika Kata za Narurango, King’ori, Majengo bado havijapata Umeme wa REA na Mkandarasi anavyofanya kazi yake wala haeleweki, analeta nguzo, anaondoka…

SPIKA: Swali!

MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO: Mheshimiwa Spika, je, ni lini Umeme wa REA utafika kwenye hizo kata ili vijiji vyote vipate umeme kulingana na ahadi ya Serikali kwamba mwisho wa mwaka huu vingepata umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. John Danielson Pallangyo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo tumetoa ahadi ya Serikali, tutahakikisha kwamba wakandarasi wote wanaotekeleza mradi wa REA III Round II kufikia Desemba mwaka huu kazi hizo zitakuwa zimekamilika katika maeneo ambayo yanapelekewa umeme kwenye kata, vijiji na vitongoji ili wananchi waweze kunufaika na hiyo huduma ya umeme ambayo iko katika huo mradi mkubwa wa mwisho wa kupeleka umeme katika vitongoji na vijiji.
MHE. EDWARD O. KISAU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri kuna tume mliunda ya kupitia vijiji vile vyenye sura ya miji hivi: Lini tume hii itamaliza kazi ili wananchi wajue wako wapi kwenye kuunganishiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa OleleKaita, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tume iliundwa na ilipita kwenye baadhi ya maeneo kukusanya maoni na tulielekeza ihakikishe inamuona kila Mbunge. Majibu yalipokuja Wizarani tulivyojaribu ku-crosscheck na Waheshimiwa Wabunge tuligundua kuna Wabunge kwa bahati mbaya hawakufikiwa na hawakuonwa na timu hii.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumeiagiza irudie upya zoezi hili kwenye yale maeneo ambayo ilikuwa haikufika na katika miezi miwili inayokuja tunaamini itakuwa imemfikia kila Mbunge na kupata maoni yake kwenye maeneo ambayo yanatakiwa kufanyiwa jitihada za kuhakikisha maeneo yenye uso wa mjini lakini ni vijijini yanapatiwa umeme kwa gharama ile nafuu. Kwa hiyo, majibu yatakapofikia mwisho tutaleta taarifa sahihi.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ninataka kujua kwa sababu viashiria vya uwepo wa mafuta kwenye Ziwa Tanganyika vimeonekana katika utafiti wa awali.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuharakisha utafiti huo ili kuweza kupata taarifa kamili?

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni lini wananchi wa Kigoma watarajie kupata taarifa za mwisho za utafiti huo ambao umechukua zaidi ya miaka mitano? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Kilumbe Shabani Ng’enda Mbunge wa Kigoma Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza katika swali la kwanza, mbinu ambazo zinafanywa na Serikali na jitihada zinazofanywa na Serikali kama mnavyofahamu Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ameifungua sana Tanzania kwa ajili ya wawekezaji, nasi Wizara ya Nishati tumekuwa tukishiriki katika maonesho mengi ya Kimataifa kwa ajili ya kuwavutia wawekezaji kuja nyumbani kufanya kazi pamoja nasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatua zinazofuata za utafiti ambazo zimebakia za 3D ni za gharama kubwa na Serikali imekuwa ikitafuta mbia wa kimkakati wa kushirikiana nae kwenye maeneo hayo ili kukamilisha utafiti huo ambao unatakiwa kufanyika. Mara tu baada ya kumpata na taarifa zikapatikana vizuri basi Ndugu zetu wa Kigoma na Watanzania kwa ujumla watapewa taarifa ya nini kimepataikana na lini uchimbaji wa mafuta katika Ziwa Tanganyika utaanza kufanyika. (Makofi)
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, Serikali wako tayari kukaa na mimi ili kuweza kufahamu hivyo vitongoji ambavyo vinaweza kunufaika na ujazilizi wa awamu ya pili unaoitwa IIC ni vitongoji gani na vingapi ili tuondoe mchanganyiko kwa sababu kuna wakati mwingine vitongoji vya Mafinga vinasomeka Mufindi na pale kuna Halmashauri ya Mji Mafinga na Halmashauri ya Mufindi. Kwa hiyo je, wako tayari kukaa na mimi ili tujue hivyo vitongoji?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; tunaipongeza Serikali kwamba maeneo ya vijijini bado wananchi wataingiza umeme kwa shilingi 27,000, lakini maeneo kama ya Mafinga yako maeneo pamoja na kuwa ni Mafinga Mji, lakini maisha, mazingira na kipato ni kama maisha ya kijijini.

Je, Serikali iko tayari maeneo kama hayo kama vile Ndolezi, Luganga na Ulole na wenyewe kuwapa bei nafuu katika kuingiza umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Chumi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wetu wa Densification 2C utakuwa na una takribani vitongoji kama 2,562. Kama alivyoomba, na mimi niko tayari, baada ya hapa nitakaanaye ili nimuoneshe vitongoji ambavyo vitakuwa ni vya eneo lake kwa ajili ya kuhudumia wananchi katika Jimbo lake la Mafinga Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye swali la pili, kama ambavyo tumeeleza siku chache zilizopita, ni kweli Wizara ilituma timu yake kwenda katika majimbo yetu yote Tanzania ili kuhakiki yale maeneo ambayo yapo mijini, lakini yana uso wa vijiji ili kuweza kuwapangia bei ambayo ni stahiki na wanayoweza kulipa. Lakini kwa bahati mbaya taarifa tuliyoipata baada ya kui-verify humu Bungeni, tulibaini kuna Waheshimiwa Wabunge hawakushirikishwa. Kwa hiyo tumeiagiza ile timu irudi tena na kwenda kubaini upya hayo maeneo na ituletee taarifa. Hivyo taarifa hiyo itakapofika tutashirikishana hapa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, tunapanga bei ambayo wananchi wataimudu kwa ajili ya kuweza kuunganisha gharama za umeme.
MHE. ALLY A. J. MLAGHILA: Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Ikombe ni kijiji ambacho kiko pembezoni sana na ni kisiwa ambacho hakifikiwi kirahisi. Leo hii tunapouliza hili swali wananchi wa Ikombe wamewatuma viongozi wao waje washuhudie majibu haya ya Serikali, wako hapa leo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ETDCO ambao wanasambaza umeme wa REA walianza kazi hii Agosti, 2021 na wamefikia vijiji 21 tu na vijiji vilivyobaki ni 14. Na katika vijiji hivyo 14 bado hata nyaya hazijavutwa wala hakujatokea uwezekano wa kupeleka nguzo na mkataba unaisha ndani ya siku kumi zijazo, swali la kwanza: -

Je, sasa Serikali haioni umuhimu mkubwa wa kushirikiana na TANESCO ili kwa Kyela vijiji hivyo viishe mapema?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni maajabu gani yatatokea kufanikisha ndani ya siku kumi mkataba huu uendelee ufike mpaka watakapofikisha hapo Juni pale Ikombe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa spirit ya kutotaja kumuwakilisha Mheshimiwa Waziri kwa ajili ya muda naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu mawali ya nyongeza la Mheshimiwa Ally Anyigulile kwa ujumla wake kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna mikataba ambayo muda wake utaisha kabla kazi hazijakamilika, lakini nia ya Serikali ni kuhakikisha kwamba vijiji vyote vinapata umeme. Na tunachokifanya ni kukabana na wakandarasi wote wanaopeleka miradi yetu ya umeme kwenye maeneo mbalimbali kuhakikisha wanamaliza kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, lakini sababu nyingine moja inayofanya kazi izidi muda wa mkataba wa awali ni kuongezeka kwa hizo kilometa mbili ambazo Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, ametoa pesa ya nyongeza kwa ajili ya kuongeza scope. Kwa hiyo, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Ally kwamba kama tulivyosema kabla ya mwezi Juni hicho kijiji kitakuwa kimepata umeme na wananchi wataweza kuutumia katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, na kwa mkandarasi ETDCO yupo zaidi ya asilimia 60 na vijiji 14 vilivyobaki vitakamilika katika huu muda ambao tumejipangia kwa spidi mpya ambayo tuko nayo kwa sasa. Ahsante.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka au kusambaza umeme kwenye vijiji na vitongoji katika Jimbo la Arumeru Magharibi ambayo imekuwa ni changamoto sana wananchi kupata umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Noah Saputi, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo mradi ambao unaendelea wa upelekaji wa umeme katika vijiji wa REA III Round Two ambao pia unahusika katika kufikisha umeme kwenye vitongji. Lakini muda si mrefu tutaanza Mradi mwingine unaitwa Densification IIC ambao una takribani vitongoji 2,600, nao ni kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji.

Mheshimiwa Spika, lakini kama ambavyo tumekuwa tukisema, tunatafuta pesa kwa ajili ya upelekaji wa umeme katika vitongoji vyote 36,000, takribani trilioni sita na bilioni mia tano ili kumaliza tatizo lolote la umeme. Kwa hiyo, nimhakikishie kwamba kwenye vile vijiji vilivyopo kwenye mradi kabla ya Desemba mwaka huu vitaisha na pesa nyingine itatafutwa kufikisha katika maeneo mengine.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo kubwa la kukatikakatika kwa umeme Wilayani Urambo, Serikali inasema nini kuhusu kumaliza ujenzi wa Kituo cha Uhuru ambacho kitakuwa ukombozi kwetu sisi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Margaret Sitta, Mbunge wa Urambo, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Kupoza Umeme cha Uhuru kilichopo katika Jimbo la Urambo kinatekelezwa katika mradi tunaouita Mradi wa Gridi Imara ambao unapokea umeme wa kilovoti 33 kutoka Tabora Mjini na mkandarasi tayari ameshapatikana ameshaagiza vifaa, na kabla ya katikati ya mwaka unaokuja tunatarajia Mradi huu wa Gridi Imara utakuwa umekamilika katika maeneo mengi likiwemo eneo la Kituo chetu cha Kupooza Umeme cha Uhuru kwa ajili ya kuhudumia wananchi walioko hapo na kupeleka Gridi ya umeme mpaka katika Wilaya ya Uvinza kupitia pale Uhuru.
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, katika Jimbo la Bunda Mjini, hasa kata saba za vijijini, kumekuwa na changamoto ya umeme kutofika kwenye nyumba za wananchi, unaishia senta: -

Je, ni lini sasa mtapeleka nguzo za kutosha ili ile dhana ya umeme vijijini iwe imekamilika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hii miradi ambayo tunaitekeleza inalenga kumfikia kila mwananchi. Lakini kwa sababu ya bajeti tuliyokuwa nayo na fedha ambayo haitoshelezi kwa wakati huu kwa maeneo yote, advancement inakwenda taratibu.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika mradi wetu wa ku-electrify vitongoji vyote ambapo tunatafuta trilioni sita na bilioni mia tano, tunaamini kwamba kila mtu atafikiwa na umeme na katika miaka mitatu, minne, mitano ijayo, hakutakuwa kuna mwananchi katika kitongoji au eneo lolote ambaye hana umeme kwa sababu hiyo ndiyo azma ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza: -

Ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata ya Ng'homolwa, Kijiji cha Nkweni?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Rose Busiga, Mbunge wa Viti Maalum Geita, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba naamini kijiji hicho na kata hiyo ipo katika mradi wetu wa REA III Round Two, na kabla ya mwaka huu kuisha kijiji hicho kitakuwa pia kimepata umeme kwenye baadhi ya vitongoji na sasa maendeleo yataendelea kwenye vitongoji ambavyo vitakuwa vimebaki.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Licha ya wananchi wa Kata ya Kibale, Kijiji cha Kigorogoro, lakini pia Businde na Lukuraijo Mkombozi kukatiwa migomba na mikahawa kwa ajili ya kuwekewa nguzo za umeme, ni zaidi ya mwaka mmoja hawajapatiwa umeme; ni lini wananchi hao watapatiwa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia Theonest, Mbunge wa Viti Maalum Kagera, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mkandarasi anayepeleka umeme katika Mkoa wa Kagera anaitwa JV Pomina Kwihaya, na yuko kazini anaendelea. Ni kweli alisuasua, katika wale wakandarasi saba ambao tulikuwa tunaona progress zao siyo nzuri na yeye alikuwemo. Lakini tumeweka strategy mpya na ninaamini Waheshimiwa Wabunge wengi wameona tumaenzisha ma-group ya whatsApp kwa ajili ya kupata updates za kila siku.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kabla ya mwaka huu kuisha umeme utakuwa umefika katika maeneo hayo kwa sababu ndiyo makubaliano yetu sisi na wakandarasi wote wanaopeleka umeme katika maeneo ya vijijini.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.

Ni lini wananchi wangu wa Kata za Pangale, Mpombwe, Tutuo, Sikonge, Mkolye hadi Ipole watapata fidia ambayo wamepisha njia ya kupita umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Awamu ya Sita inajenga laini ya kilovoti 33 ya kupeleka Gridi ya Taifa Katavi ambapo inatokea Kituo chetu cha Tabora inapita Ipole ambako ndiko katika jimbo lake, inakwenda Inyonga na baadaye inafika Mpanda Mjini.

Mheshimiwa Spika, laini yote hiyo ina jumla ya kilometa
380 na pesa zimeshapatikana kwa ajili ya kulipa fidia, na mkandarasi anaingia site karibia kwenye mwezi Julai au Agosti. Kabla ya muda huo fidia itakuwa tayari imelipwa ili Gridi ya Taifa iweze kufika Katavi na wananchi wake wataweza kulipwa fidia ambayo wanastahili kupewa.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kawekapina, Ipululu na Vumilia Kata ya Igalula wanacheleweshewa kupata umeme kwa sababu ya mgogoro wa TANESCO, TRC na REA: -

Je, ni lini mtaumaliza mgogoro huu wa kuvusha nyaya kwenda kwenye vijiji hivyo ili wananchi wapate umeme kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Venant, Mbunge wa Igalula, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, TANESCO na REA wako tayari na wanayo fedha kwa ajili ya kuvusha umeme kwenye line ya SGR lakini wenzetu wa Wizara ya Uchukuzi walikuwa hawajajua eneo gani watuoneshe kwa ajili ya kupitisha njia na sisi tusingependa tutumie pesa nyingi kupisha eneo temporary halafu baadae kidogo tuhamishie kwingine. Tumekaa pamoja na wenzetu wa TRC watatuonesha sehemu ambayo ni ya kudumu tutakayopitisha miundo mbinu hiyo ili wananchi waweze kupata umeme katika maeneo hayo. Kwa hiyo nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba tunalifatilia na tutalikamilisha kwa wakati ili wananchi waweze kupata huduma.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niulize maswali mawili ya nyongeza kwa niaba ya Mheshimiwa Tauhida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; kwa kuwa mpango huu wa Serikali umekuwepo kwa siku kidogo lakini bado ulipaji wa madeni umesuasua. Je, ni mikakati gani ya dharura ambayo Serikali itachukua kuhakikisha kwamba ulipaji unafanyika kwa uharaka na kwa ufanisi zaidi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa bilioni 244 ni pesa nyingi sana inazodai Serikali, je, Serikali ina mikakati gani ya kisheria ambayo itachukua kuhakikisha kwamba hizi pesa zinalipwa kwa kuwapeleka hawa watu Mahakamani au kwa njia nyingine yeyote, lakini pesa hizi zilipwe ambazo ni muhimu sana kwa maendeleo ya shirika na nchi yetu kwa jumla?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Asha Abdullah Juma kwa pamoja, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme hizi pesa bilioni
244 kwa sehemu kubwa ni deni la nyuma na ni deni la siku nyingi. Ni deni ambalo lilikuwepo kipindi kile ambacho bado tulikuwa hatujaanza kutumia LUKU na tulikuwa hatujaweza kukusanya vizuri. Kwa hiyo ni madeni ya siku nyingi na tunaendelea kuhangaika nayo kama ambavyo Mheshimiwa amesema tuna mkakati gani wa kuhakikisha kwamba tunayakusanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mikakati iliyopo ya kukusanya pesa hizi kwanza ya dharura kabisa tayari TANESCO imeshakamilisha taratibu za kuwapata madalali wa kukusanya madeni wawili ambao taratibu zinakamilishwa na siku siyo nyingi wataanza kuingia mtaani na kukusanya fedha hizi ambazo ziko kwa watu mbalimbali ili kuweza kuzipata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili upande wa Serikali, Wizara na TANESCO tumeshirikiana na kuiomba Serikali kupitia Hazina ilipe pesa hii yote inayodaiwa kwa TANESCO ili TANESCO iweze kupata fedha ya kuweza kujiendesha. Sasa kwenye mikakati inayokuja ya nini kinafanyika pamoja na hizi LUKU ambazo tumeshaweka, lakini zinawekwa LUKU zinaitwa boundaries meters ambazo zitawekwa kwenye ngazi ya Mkoa ili kila Mkoa tujue inatumia umeme kiasi gani. Pia tunakwenda kwenye kuweka smart meters ambazo zitatusaidia kujua mtu anapogusa meter yetu moja kwa moja tukiwa ofisini tutaiona na kuhakikisha kwamba tunashughulikia suala hilo mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mahakama, tusingependa tufike huko mapema kwa sababu Mahakama inachukua muda mrefu na process nyingi, lakini wale wateja ambao tunashindwana kabisa hata zile hatua za kukata umeme, basi tunapelekana Mahakamani. Zipo kesi kadhaa ambazo tumeenda Mahakamani na tumeshinda na tuna uhakika kwamba deni hili tutalikusanya lote ndani ya muda mfupi.
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Taasisi ambazo zinaongoza kudaiwa deni na TANESCO ni Taasisi za Serikali tena zile andamizi, za binafsi either hamna kabisa au ni moja, mbili au tatu, nataka kujua sasa kwa sababu kuna Taasisi zingine zinatoa huduma kwa wananchi, haziwezi kukatiwa umeme. Je, ni kwa nini Serikali isiweke pre- paid meter kwa hizi Taasisi zote ili ziweze kuwajibika na kuona kipaumbele cha kwanza cha ku–fine kuweza kulipia umeme kuliko hivi sasa kuweza kuleta usawa kati ya wananchi na hizi Taasisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hii bilioni 244 Serikali inadaiwa kama bilioni 86 hivi kwa hiyo bilioni mia moja ishirini na kitu zinazobakia wateja binafsi na watu mbalimbali ndiyo wanaodaiwa. Hao wateja binafsi ni wale wateja wadogo wadogo na kama nilivyotangulia kusema, madeni haya hasa ni ya kipindi kile ambapo hatukuwa na meter.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa utaratibu tunaokwenda nao tumeshaongea na wenzetu Serikalini kukubaliana kwamba pesa inayolipwa kwenye zile taasisi kwa ajili ya kulipia huduma ya umeme, hii ya deni ikatwe at source kwa maana ya kutoka Hazina, lakini hizi pesa nyingine zinazokuja basi tuweke utaratibu mzuri ambazo tutaweza kuzikusanya. Pre paid meters na na hizo smart meters zinazokuja tutahakikisha tunazi–roll kwenye maeneo yote ili kila mmoja aweze kuwa na wajibu wa kulipa deni lake kwa wakati tukihakikisha kwamba sasa ni kwa manufaa yetu sisi wazalishaji na watumiaji wa umeme tunaozalisha.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Moja ya changamoto kubwa inayopelekea miradi hii ya REA kutotekelezwa kwa wakati ni pamoja na ukosefu wa nguzo. Nataka kusikia kauli ya Serikali imejipangaje kwa ajili ya kutatua changamoto hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa kuna makampuni yasiyo na uaminifu katika kutekeleza miradi hii ya REA jambo ambalo linasababisha kuendelea kuchelewesha utekelezaji wa miradi hii, mfano kampuni ya TONTAN ambayo imetumia zaidi ya bilioni 3.8 kinyume na utaratibu. Nataka kujua kauli ya Serikali imekwishachukua hatua gani mpaka sasa dhidi ya kampuni hii?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la nguzo kwa ajili ya usambazaji wa umeme tunaendelea kuvihamasisha na kuviwezesha viwanda vyetu vya ndani kuhakikisha kwamba vinatosheleza soko. Hata hivyo, ni kwa sababu kazi zimekuwa nyingi na miradi imekuwa mingi na hivyo viwanda vinaonekana kuzidiwa na kazi ambazo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amewezesha zifanyike katika nchi yetu. Hata hivyo, tunajitahidi na viwanda vimekuwa vikizalisha nguzo na kwa sehemu kubwa tatizo huilo limepungua na endapo litakuwa kubwa sana tutahakikisha tunazipata kokote zinakowezekana kupatikana ili hilo tatizo liishe.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili, kuhusiana na wakandarasi ambao wanalegalega katika katika utekelezaji wa kazi zao. Kama ambavyo tumekuwa tukisema tunao wakandarasi wa lot kama saba ambao tumekuwa tukikamatana nao kwa nguvu zaidi kuhakikisha kwamba wanakamilisha kazi zao. Vile vile, tumewekeana malengo na mikakati na muda utakapofika endapo watashindwa kukamilisha, basi tutavunja mikataba hiyo ili tuweze kupata watu wengine wa kukamilisha kazi kwa wakati. Hata hivyo, kwa sasa tunaendelea vema katika ambayo tumeweka utaratibu wa kufuatilia siku kwa siku kwa kuajiri wale vijana wetu ambao tumewapeleka katika maeneo yetu ya majimbo na hivyo tunapata taarifa za mara kwa mara na usimamizi unakuwa wa karibu. Tunaamini kazi zitakamilika kwa wakati.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Wilaya ya Namtumbo tuna Vijiji viwili cha Ligunga na cha Msisima chenye Shule ya Sekondari ya Kata ya Msisisima iliyojengwa kwa gharama ya shilingi milioni 600, kilirukwa katika awamu hii na awamu ya tatu mzunguko wa pili. Vile vile, tuliomba viingizwe na vikapata proof na mkandarasi amefanya survey ameleta…

SPIKA: Mheshimiwa swali lako.

MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Spika, je, Serikali lini itampa kibali aendelee kufanya kazi hiyo ya kuweka umeme katika Kijiji cha Msisima na Ligunga?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme vitawekewa umeme na mikataba tuliyokuwa nayo inaisha Desemba, 2023, vile vilivyokuwa kwenye miradi ya awali na vile ambavyo vilikuja kuongezwa vyote vitafanyiwa kazi kwenye scope hii ambayo tunakwenda nayo na vitakamilika katika awamu hii.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii. Jimbo la Newala Vijijini lina vijiji zaidi ya 60 ambavyo havijapatiwa umeme. Je, ni lini Mradi wa REA, mzunguko wa pili, utaenda kumaliza tatizo hili? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, Mradi wa REA, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, unaendelea na tunatarajia utakamilika ifikapo Desemba, 2023. Katika Jimbo la Newala Vijijini napo mradi huu utatakiwa ukamilike na vijiji vyote vilivyopo vitapata umeme.
MHE. HASSAN Z. KUNGU: Mheshimiwa Spika, nakushuru. Kutokana na mpango wa umeme vitongojini kwa Wilaya ya Tunduru bado haujaanza na kuna taasisi mbili za kidini ambazo hazina umeme na ziko vitongojini. Je, ni lini Serikali itapeleka huduma ya umeme kwenye taasisi hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, tayari Serikali ya Awamu ya Sita ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, imetoa fedha za nyongeza za kupeleka umeme katika kilometa mbili za ziada ukiachana na ile moja ambayo tulikuwa nayo katika Mradi wa REA III Round II. Kwa hiyo, naamini katika nyongeza hiyo ya kilomita mbili itazidi kuingia kwenye maeneo ya vitongoji na taasisi hizo zikiwekwa ni za kipaumbele, basi Mkandarasi atafikisha umeme kwenye maeneo hayo kwa kipindi hiki ambacho tumepata nyongeza ya pesa ya kupeleka umeme katika kilomita mbili za ziada ukijumlisha na ile moja ambayo itagusa vitongoji vingi zaidi.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika shule zote za msingi, sekondari na taasisi za dini katika wilaya zote Mkoa wa Kigoma?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, katika mpango wa REA III, Round II, tuliokuwa nao sasa tunafikisha umeme katika vijiji vyote na katika maeneo ya vitongoji baadhi kwa kilomita moja ukiongeza na zile kilomita mbili. Hata hivyo, tayari Serikali inatafuta fedha ya kuhakikisha inapeleka umeme katika vitongoji vyote Tanzania takribani 36,000 ambavyo havina Umeme kwa gharama ya shilingi 6,500,000,000,000. Pesa hiyo itakapokuwa imepatikana taasisi na maeneo mengine yote yanayohitaji umeme yatafikishiwa umeme kulingana na upatikanaji wa fedha ambao tunaamini zitapatikana katika muda mfupi ujao.
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza.; je, ni vigezo gani vinatumika kupanga ugawaji wa umeme kwa urban peri -urban pamoja na REA?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; ni upi mpango wa Wizara katika kushughulikia malalamiko ya wananchi juu ya tariff kwa bei za umeme kuwa kubwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Esther Malleko, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la kwanza, TANESCO imekuwa ikipanga Mradi wa REA uende wapi na Peri-Urban uende wapi kulingana na taarifa zinazotolewa na TAMISEMI. Pia wenzetu wa TAMISEMI ndio wenye dhamana ya kusema hapa ni mjini na hapa ni kijijini, hapa ni Halmashauri ya Mji, hapa ni Jiji na hapa ni Manispaa. Kwa hiyo, sisi TANESCO tumekuwa tukipata taarifa za TAMISEMI na tunatumia hizo kupeleka Miradi ya Peri-Urban kwenye maeneo ya mijini na Miradi ya REA kwenye maeneo ya vijijini. Pia tumeendelea kushirikiana nao kubaini maeneo jinsi yanavyobadilika ili tuweze kufikisha huduma sahihi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili, katika hizi nchi za jirani na Tanzania, watu wenye bei za chini kabisa za umeme ambazo kimsingi kabisa zimewekewa ruzuku na Serikali ni Tanzania. Gharama za uzalishaji na usambazaji wa umeme Tanzania haziko na usawa na uwiano sahihi na gharama zinazolipwa na wananchi katika kupata ile huduma ya umeme na kuunganishwa. Kwa hiyo, gharama zetu ziko chini na sisi tunadhani kuna haja ya kuzitazama vizuri ili shirika liweze kuendelea kujiendesha na kuweza kutoa huduma sahihi kwa wananchi na kwa wakati.
MHE. DKT. CHRISTINE C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Serikali iliahidi kuvipatia umeme vijiji vilivyopo katika Kata ya Mwamalili, Kolandoto, Chibe, Mwawaza na Old Shinyanga; je, ni lini Serikali itavipatia umeme vijiji hivyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Viti Maalum, Shinyanga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote ambavyo havikuwa na umeme na havina umeme hadi sasa viko katika Mradi Mkubwa wa Umeme wa REA, awamu ya tatu, mzunguko wa pili. Kufikia Desemba, 2023 tuna uhakika vijiji hivyo vitakuwa vimepata umeme kupitia mikataba ambayo tuko nayo na inayoendelea kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huo ndio tunamshukuru Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuongeza kilomita mbili katika ile kilomita moja tuliyokuwa nayo awali. Kwa hiyo wigo wa mradi utakuwa ni mpana zaidi kuweza kuwafikia wananchi wengi katika vitongoji kwa ajili ya kupata maendeleo kwenye maeneo yao.
MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Naibu Spika, naishukuru Serikali kwa kuwasha umeme kwa wakati katika vijiji vya Jimbo la Meatu hususani kwenye kata ambazo zilikuwa hazijaguswa. Je, ni lini sasa Serikali itaanza kusambaza umeme wa ujazilizi katika vitongoji vyote vya Jimbo la Meatu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Leah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza tunashukuru kwa pongezi angalau kuna maeneo ambapo Mradi wetu wa REA III, round II umekamilika ikiwemo Mkoa wa Simiyu na tunaendelea kuhakikisha kwamba na maeneo mengine mradi unakamilika. Katika vitongoji kama nilivyotangulia kusema tayari tumepata fedha kwa ajili ya kuongeza wigo kutoka kilomita moja hadi kilomita tatu ambazo zitafika katika vitongoji vingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali inatafuta fedha nyingi zaidi za kuweza kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote takribani 36,000 ambavyo vimebaki Tanzania visivyokuwa na umeme takribani shilingi 6,500,000,000,000 na tunaamini zitapatikana na umeme katika miaka minne, mitano au sita ijayo, vitongoji vyote Tanzania vitafikiwa na huduma ya umeme.
MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipatia nafasi ya kuulizwa maswali mawili ya nyongeza.

Swali langu la kwanza, je, ni kiasi gani GST imewezeshwa kufanya kazi?

Swali langu la pili, je, Serikali ina mpango gani mahsusi kuhakikisha Watanzania wananufaika na madini haya yanayopatikana nchini Tanzania? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Kainja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la kwanza GST katika bajeti hii ambayo ilipitishwa na Wizara ya Madini imetengewa kiasi cha fedha shilingi bilioni mbili na milioni mia nne kwa ajili ya shughuli zake mbalimbali ikiwemo kipande kidogo kwa ajili ya utafiti.

Mheshimiwa Naibu Spika, shughuli hizi za utafiti zinahitaji fedha nyingi sana kwa hiyo shilingi bilioni 2.4 peke yake haitoshi, wenzetu wa GST tayari wameshaanza kufanya proposal za kupata fedha kutoka maeneo mengine ili kuweza ku-complement kwenye zile fedha ndogo ambazo wanazo kwa ajili ya kukamilisha hii kazi ambayo wamepatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu swali la pili ni mkakati wa Serikali ambao unafahamika wazi kwamba madini yanayochimbwa Tanzania yanawanufaisha Watanzania wote, uniruhusu nitoe mfano mmoja kwa juzi Barrick imetoa CSR kiasi cha shilingi bilioni 30 ambayo kwa kuanzia imetoa Shilingi Bilioni 10, hata sisi ambao hatuko katika yale maeneo ya mgodi tumepata fedha hiyo. Kwa hiyo, Watanzania wote Serikali imeweka mpango wa kuhakikisha kwamba kila mmoja anayetakiwa kunufaika nayo ananufaika kwenye eneo lake.
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaja na swali la nyongeza kwanza nisikitike kwa majibu ambayo hayajaridhisha. Hayajaniridhisha mimi wala wananchi wa Liwale. Nina sababu zifuatazo; kwanza Wizara haikuzingatia umbali uliopo kutoka Liwale kwenda Nachingwea lakini vile vile haikuzingatia miundombinu ya usafiri uliopo kutoka Liwale kwenda maeneo iliyotajwa. Hata Mkoa wenyewe wa Lindi ukiuangalia ukubwa wake Wilaya ya Liwale ndiyo yenye eneo kubwa Mkoa wa Lindi. Takriban theluthi moja ya Mkoa wa Lindi iko Liwale. Sasa kuniambia kwamba Wilaya ya Liwale ina shughuli pungufu ya uchimbaji wa madini napata shida kukubaliana na jambo hilo. Hii ni kwa sababu kuna eneo kubwa sana ambalo linazungumzwa Wilayani Nachingwea, eneo la Kitowelo. Eneo hili la Kitowelo liko mpakani na Liwale...

MWENYEKITI: Mheshimiwa uliza swali la nyongeza.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Swali langu: -

(a) Je, Wizara hii ya Madini haiko katika mfumo ule wa kusogeza huduma kwa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana kama ingekuwa kwenye hiyo mpango wa kusogeza huduma kwa wananchi kwa karibu basi na sisi tungepatiwa Ofisi. Ile taasisi ya GST ilikuja Liwale ikakaa mwezi mzima ikakaa pale Liwale waliweka kambi Mpigamiti pale, mwezi mzima. Wamefanya utafiti wa madini lakini mpaka leo hatujapata sisi kama Wilaya, kupata hata kile kitabu cha matokeo yale ya uchimbaji wa madini. Matokeo yake sasa watu kutoka Kanda ya Ziwa ndio wanachukua vitalu kule kwa wingi sana kwa sababu matokeo yote yako hapa GST Makao Makuu.

(b) Je, Wizara ya madini iko tayari sisi kama Halmashauri kutupatia vile vitabu vya matokeo ya utafiti ule?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI K.n.y. WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kuchauka, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza, Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan ni Serikali ya wananchi, na nia yake kubwa ni kupeleka huduma kwa wananchi. Kama tulivyosema kwenye jibu la msingi, ni kwamba, ofisi zitafunguliwa kulingana na Wingi na uhitaji wa ofisi hizo kwenye maeneo hayo. Lakini pia nimemalizia kwa kusema Wizara itaendelea kuboresha huduma kwa wadau wake kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimuhalkikishie Mheshimiwa Kuchauka, mpaka sasa Tanzania ina masoko 42 ya kununua na kuuza madini, ina vituo 93. Kadri maeneo yanavyozidi kuongezeka na uhitaji unavyotokea huduma hii inazidi kusogezwa kwa wananchi. Hata katika Jimbo la Liwale watakwenda kutizama na kuona wingi na upana wa mahitaji ya ofisi hizi, na zitapelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili; nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge; wananchi wa Liwale niliwashauri kutembelea ofisi za madini watapata hizo taarifa za madini yaliyopo kama ambavyo anasema, kwamba waliotoka sehemu za mbali wamepata taarifa hizo. Lakini pia ofisi itahakikisha inatoa taarifa hizo kwa sababu si za siri, kwa wananchi, ili waweze kuzi-access na kuweza kuingia kwenye maeneo hayo kuweza kuchimba madini ili kunufaika nayo. Sisi sote tunaohitaji kunufaika nayo.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri sana ya Serikali, pamoja na hivyo bado naomba kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Sera ya Taifa inaeleza kwamba maeneo ya pembezoni mwa Miji na Manispaa yatakwenda kuwekewa umeme kwa gharama ya shilingi 27,000 na siyo shilingi 300,000 kama ilivyo sasa.

Je, ni kwanini Serikali inakwenda kinyume na sera yake yenyewe? (Makofi)

Swali la pili, je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye Kata zenye mazingira ya vijijini ambazo ni Rilambo, Shibira, Dilimalitembo, Mletele, Shule ya Tanga, Mwengemshindo, Mbati na Wenje? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza la kuhusu bei ya shilingi 27,000 kwenye sera, naomba kuliarifu Bunge lako kwamba bei zinazotumika kuunganisha umeme kwa wateja wa TANESCO zinapangwa na kusimamiwa na Mamalaka ya Udhibiti ya EWURA. Kwa hiyo, kinachofanywa ni kuangalia maeneo maalum na kuyapangia bei yake. Maeneo ya vijijini ni shilingi 27,000 maeneo ya mijini ni shilingi 321,000 na kuendelea.

Mheshimiwa Spika, ilijaribiwa kufanyiwa shilingi 27,000 kila sehemu lakini kwa uhalisia ilionekana ni ngumu, lakini zoezi la kuendelea kubaini ni kiasi gani kitumike kuunganisha eneo gani kinaendelea kama ambavyo tumekuwa tukitoa taarifa na jambo hilo litakapokamilika basi bei nzuri za kila eneo zitatangazwa ili ziweze kutumika.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili. Kuhusu umeme kupelekwa katika maeneo ya vijijini lakini yaliyoko mijini tunafanya hivyo, kwenye baadhi ya maeneo tayari kuna awamu ya kwanza ilishafanyika kwa Mikoa kadhaa, awamu ya pili imefanyika na sasa inaendelea awamu ya tatu. Nimhakikishie Mheshimiwa Msongozi kwamba katika maeneo aliyoyataja nayo yamo katika plan za Serikali na upatikanaji wa fedha utakavyokuwa tayari maeneo hayo pia yatapelekewa umeme katika maeneo ya mijini yenye uso wa vijijini kwa kadri ya upatikanaji wa fedha katika siku chache zijazo. Nashukuru.
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kutokana na tatizo kubwa la umeme tulilonalo Wilayani Urambo, ni lini kituo kinachojengwa Kata ya Vumilia eneo la Uhuru litakamilika kama utatuzi wa tatizo hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, Kituo cha Uhuru kilichopo Urambo ni mojawapo ya vituo 14 vinavyojengwa katika mradi wetu wa Gridi Imara na kabala ya mwaka huu kuisha kituo hicho kitakuwa kimekamilika kwa sababu tayari mashineumba (transformer) zimeshakaguliwa kiwandani na sasa zimefungwa kwa ajili ya kuja kuwekwa katika kiwanda hicho kwa sababu jengo tayari lilishakamilika na lane inaendelea kujengwa.

Mheshimiwa Spika, hivyo, kabla ya mwaka huu kuisha kitakuwa kimekamilika ili kuweza kuhudumia wananchi. (Makofi)
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mkoa wa Kigoma unaunganishwa katika Gridi ya Taifa, mpaka sasa Wilaya za Kigoma na Uvinza bado hazijaunganishwa. Je, ni lini Serikali itakamilisha kazi ya kuunganisha Wilaya hizi ili kukamilisha Mkoa wa Kigoma? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Kigoma umeunganishwa kwa Gridi ya Taifa kwa line ndogo inayotoka katika kituo chetu cha kupoza Umeme cha Nyakanazi na line hiyo ya msongo wa kilovolti 33 iliishia maeneo ya Kibondo, lakini tayari mradi mkubwa wa kilovolti 400 unaojengwa kutoka Nyakanazi kwenda Kidahwe Mjini Kigoma wa kilometa 280 unaendelea, kabla ya mwaka 2025 utakuwa umekamilika na hivyo Mkoa wote wa Kigoma utapata huduma ya umeme wa Gridi ya Taifa.
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana ninayo maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Manyoni inapata umeme kutoka Singida na kutoka Singida – Ikungi – Manyoni lakini Itigi – Mitundu hadi Mwamagembe, kutoka kituo kikubwa kinachopoza umeme ni karibu kilometa 400. Serikali ilikuwa na mpango wa kujenga vituo vya kupoozea umeme substation katika Mkoa wa Singida ikiweo Iramba na hiki cha Manyoni ambacho amekitaja kwenye majibu na cha Mitundu.

Je, ni lini sasa wanaenda kujenga vituo hivi katika Mkoa wa Singida? (Makofi)

Swali la pili, nguzo za zege sasa hivi tunaziona katika maeneo mengi zikiwekwa, njia hii ndefu ya kutoka Singida kama nilivyoitaja na umbali wake kutoka Manyoni lakini kutoka Itigi kwenda Mitundu mpaka Mwamagembe kilometa ni nyingi. Ni lini wataweza kuweka sasa nguzo za zege kwa sababu maeneo haya kuna maeneo chepe chepe, maeneo ya misitu lakini maeneo yenye acid yanakula sana nguzo hizi za miti.

Je, ni lini sasa Serikali itaanza kufanya hilo zoezi ili kufanya maisha yawe mazuri, umeme ni maisha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mojawapo ya sababu ya umeme kukatika katika maeneo mengi ni kusafiri kwa umbali mrefu. Serikali kupitia TANESCO ilifanya upembuzi yakinifu na kubaini mahitaji ya vituo vya kupooza umeme takribani 88 katika Halmashauri zetu zote, imetafuta fedha kupitia mradi wetu wa Gridi Imara na tukapata karibia shilingi trilioni nne na shilingi bilioni mia mbili ambazo zitakuja kwa awamu nne. Awamu ya kwanza tumepata shilingi bilioni 500 na tutajenga vituo 15 katika Wilaya mbalimbali. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Massare pamoja na Waheshimiwa wengine kwamba itakapofika miaka mitano, sita ijayo baada ya mradi wa Gridi Imara kukamilika, kila wilaya tunatarajia iwe na kituo cha kupoaza umeme ili umeme usisafiri umbali mrefu na kuweza kukatika katika humo njiani.

Mheshimiwa Spika, sasa vituo alivyovitaja vya Iramba, Mkalama na maeneo mengine vitajengwa pia katika awamu hizo kulingana na wale ambao wana hali ngumu zaidi kufuatia wenye hali nzuri kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la nguzo za zege ni kweli Serikali inafanya jitihada za kuhakikisha inabadilisha nguzo za miti kuweka za zege katika maeneo chepe chepe, yenye wadudu waharibifu na maeneo ya mapori ambapo hatuwezi kuingia mara kwa mara kufanya marekebisho. Maeneo aliyoyasema ni ya kipaumbele na tutaenda kuyatazama ili tuyaweke kwenye mpango wa kuyabadilishia kutoka nguzo za mbao kuweka za zege ili umeme upatikane kwa wakati wote katika maeneo hayo na maeneo mengine pia. Ninakushukuru.
MHE. NDAISABA G. RUHORO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nimefurahishwa na majibu ya Serikali nina swali moja la nyongeza. Kwa kuwa eneo lile la Rusumo limewahi kukumbwa na majanga ya moto hasa eneo lile ambalo bwawa lenyewe limejengwa. Na kwa kuwa ulipotokea moto tulilazima kuomba ndege ya kuzima moto kutoka Taifa Jirani. Ni upi mkakati wa Wizara wa kuhakikisha tunakuwa na gari la zimamoto ili kulinda miundombinu yetu tuliyowekeza pale, pale itakapotea majanga ya moto kama ilivyotea huko nyuma? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nishukuru kwa niaba ya Serikali kwa kufurahishwa na majibu haya na ukamilikaji wa mradi. Nimpongeze Mheshimiwa Mbunge kwa kufatilia mradi wote lakini hasa suala la kuzima moto. Nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inalichukua tunaamini mradi utakapo kamilika kuna serving ambayo itatafanyika. Tutahakikisha basi tunawashawishi ili waombe katika mahitaji yao muhimu ya matumizi ya ile pesa itakayobaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia katika Miradi ya CSR ambayo itaanza kufanyika baada ya mradi kukamilika tutawashauri pia walilete kama moja wapo ya hitaji lao ili tuweze kulifanyia kazi na Serikali itahakikisha kwamba linafanyika kwa ajili ya ku–safe guard maisha ya watu wanayo tumia maeneo hayo.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri nawashukuru sana Wizara ya Nishati, mmeleta pale vijiji 33 kutengeneza umeme kilometa mbili mpaka kilomita tatu na sasa Mkamburo Mkandarasi atengeneze kilometa moja tu na ameleta mzozo mkubwa kwa wananchi wale waliyopimiwa mara ya kwanza kuwaonyesha kwamba ni kilomita mbili. Ni lini sasa mtaongeza hizo kilomita mbili au tatu zilizokuwa zimepungua kutoka kilometa tatu mlizokuwa mmeongeza zamani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, tayari tunaendelea kukamilisha mikataba ya kuongeza kilomita mbili kwa kila kijiji kutoka kwenye ile kilomita moja ambayo ilikuwa inafanyika katika ya awamu ya tatu mzunguko wa pili wa REA.

Mheshimiwa Naibu Spika, siku siyo nyingi wakandarasi wale ambao wameonekana wakikidhi kufanya vizuri miradi hii ya REA three round two watakuja site kuonyeshwa hizo kazi za nyongeza. Wale ambao wameonekana wakilegalega tutahakikisha tunapata wengine ili waje wafanye hiyo kazi na kuikamilisha yote kwa pamoja.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi Kata ya Mamboya katika Jimbo la Kilosa maeneo mengi hakuna umeme. Nini mpango wa Serikali kuweka umeme katika maeneo hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumeeleza mara kwa mara hapa Bungeni ni azima ya Serikali wa Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan kuhakikisha kwamba kabla kabla ya Desemba, 2023 vijiji vyote vimepata umeme. Naamini katika kata hiyo waliyoitaja vijiji vilivyomo ambavyo havijapata umeme vinakuwa vimepata umeme kabla ya mwezi Desemba kuisha mwaka huu.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante Wilaya ya Makete mmetupatia mradi wa ujenzi wa Bwawa la Umeme la Rumakali mmeishafanya demarcation, mmeifanya tathimini ni takribani miezi mitano toka mmefanya hivyo amjaanza kulipa kwa maana kuwalipa wafanyakazi wale. Muda huu wananchi wa Makete wanawasikiliza ni lini Serikali itawalipa wananchi wanaozunguka bwawa hilo ili waachane na shughuli za kilimo na za kiuchumi zilizoko pale waanze kufanya shughuli zingine? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikweli Serikali ya Awamu ya Sita inayo dhamira ya kujenga Mradi wa Rumakali wa kuzalisha megawati 222 kwa kutumia nguvu ya maji. Kama alivyosema Mheshimiwa Festo tayari tumeishafanya upembuzi yakinifu na tathimini ya site imeishafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kinachotarajiwa sasa ni mwezi unaofuata wa sita wananchi wataenda kuonyweshwa nani atalipwa shilingi ngapi, ili kwenye mwaka wa fedha unaokuja kuanzia Julai fidia hiyo iweze kufanyika. Kwa hiyo, wananchi wawe na subiri kidogo ndani ya miezi miwili, mitatu fidia yao itaanza kulipwa kwa ajili ya kupisha maeneo ya mradi.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu ya Serikali, nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza. Serikali inatoa kauli gani ya kutatua changamoto ya umeme mdogo (low voltage) katika Wilaya ya Buhigwe wakati mkandarasi anaendelea na kazi? (Makofi)

Mheshimwa Mwenyekiti, swali la pili. Pamoja na kwamba Gridi ya Taifa imeshaifikia Wilaya ya Kankonko, Kibondo, Kasulu na Buhigwe, bado taasisi za Serikali kama shule, taasisi za kijamii (misikiti, makanisa) pamoja na vitongoji havijapata umeme: Lini Serikali itapeleka umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la umeme hafifu (low voltage) ambalo ameliataja, ni suala la kawaida katika matumizi ya umeme na linatokea pale ambapo watumiaji wanakuwa wengi katika eneo husika, na hivyo vifaa vyetu kuzidiwa. Ni suala kama la kufanya service ya magari. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba TANESCO na Serikali tayari tumetenga fedha kuhudumia maeneo yote yenye matatizo ya low voltage kwa kuongeza vitu vinavyoitwa auto- voltage regulatora na pia kwa kuweka transformer kubwa ili kuweza kusuka umeme mwingi na kuwafikia wahitaji. Katika maeneo anayoyasema nitawasiliana naye ili tujue maeneo mahususi, tuone hatua zilizochukuliwa na zilizofikiwa katika kutatua tatizo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, ni kweli kwamba Desemba mwaka huu tunatarajia kukamilisha vijiji vyote, lakini tutatafuta fedha kwa ajili ya kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote nchini na taasisi zote alizozisema zikiwemo shule, makanisa na maeneo mengine yatapelekewa umeme kufuatia kupatikana kwa fedha, takribani shilingi trilioni tano au sita kwa ajili ya kumaliza maeneo yote yanayohitaji umeme yakiwemo maeneo ya Buhigwe na maeneo mengine ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nisikitike sana kutokana na majibu ya Naibu Waziri, haya majibu sidhani kama wanafanya research. Manati, watoto wanapiga vikombe kweli? Ni kitu cha kushangaza sana, lakini sasa kinachonishangaza zaidi kwenye chanzo cha umeme ndiko kwenye shida kubwa ya umeme. Je, ni lini Serikali itatuhakikishia kwamba huku tunapata umeme wa uhakika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikilalamika hapa kila siku kuhusiana na Jimboni kwangu Lulindi. Mkandarasi alipewa vijiji takribani 30 kushughulika na umeme kwa maana ya viunganishi, hakushughulikia hata kijiji kimoja, nimekuwa nikiimba kama wimbo. Je, ni lini nitaacha kuja hapa kulalamika kuhusiana na suala la umeme jimboni kwangu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyomalizia paragraph ya mwisho; upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa Mkoa wa Mtwara utatokana na kukamilisha hizi njia mbili ambazo zinaleta umeme wa gridi ya Taifa kutoka katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna tatizo kwenye njia ya umeme, hata kama ni kwenye eneo la chanzo umeme utakatika. Kwa hiyo, azma ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha kwamba, miundombinu yote hii inarekebishwa na kuimarishwa, ili iweze kusafirisha umeme kwa wakati wote na kuwafikia wale walengwa ambao wanatakiwa kuutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la pili; mkandarasi anayetekeleza miradi ya REA katika eneo la Lulindi ambalo ni Masasi, ana Wilaya ya Masasi na Nanyumbu, anaitwa Namis, alikuwa katika wale wakandarasi wenye lot zile saba ambazo zilikuwa zinasuasua, lakini tumesukumana naye na kuwekeana masharti na tunaamini kufikia Disemba na yeye atakuwa amekamilisha kazi yake. Kwa Lulindi alishawasha vijiji kama sita au saba kutoka kwenye vile alivyokuwanavyo na tunaamini kabla mkataba haujaisha atakamilisha kazi kwa sababu, tunasimamiana naye kwa karibu sana.
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza. Kupitia Bunge hili tuliahidiwa kwamba, umeme wa Makete watabadilisha line kutoka Mbeya kuja Makete ni line ambayo inasumbua na imechoka kwa muda mrefu na inasababisha umeme Makete kukatika mara kwa mara. Wakatuahidi kwamba, watajenga substation Wanging’ombe ili wananchi wa Makete tuchukue umeme kutoka Njombe. Je, hatua hiyo imefikia wapi ili wananchi wa Makete wanaosikiliza sasa hivi wapate uhakika wa majibu ya Serikali? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya changamoto ambayo tumekuwa nayo ni umeme kusafirishwa umbali mrefu kutoka kwenye chanzo. Tulifanya tathmini kupitia TANESCO na tukabaini makundi matatu, kuna wale ambao wana shida zaidi, kuna wenye shida za kati na kuna wale ambao maisha yanaweza yakaendelea.


Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwenye maeneo yenye shida zaidi tunaishukuru Serikali ya Awamu ya Sita imetupatia pesa bilioni 500 kwa ajili ya kutekeleza Mradi unaitwa Gridi Imara na utajenga vituo vya kupoza umeme 14 katika awamu hii ya kwanza. Sasa nimhakikishie Mheshimiwa Festo kwamba, eneo lake nitaenda kuliangalia limewekwa kwenye category ipi katika yale maeneo matatu yenye matatizo makubwa, matatizo ya kati na matatizo ya juu na nitamfahamisha endapo kitajengwa kituo cha kupoza umeme kipindi hiki au kitajengwa katika awamu inayofuata, lakini kabla ya miaka sita ijayo kwisha tunatarajia kuwa na kituo cha kupooza umeme kwa kila wilaya ili kuondoa matatizo ya umeme kusafirishwa kwa muda mrefu.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Wilaya ya Ngorongoro tangu iunganishwe na Gridi ya Taifa mwaka jana tatizo la umeme limezidi kuongezeka. Gridi ile iliunganishwa kutoka Wilaya ya Longido, ikitokea hitilafu ya umeme katika Wilaya ya Longido, Ngorongoro wanakosa umeme, ikitokea hitilafu Ngaramtoni, Ngorongoro wanakosa umeme na ikitokea hitilafu wilayani kwao wanakosa umeme. Imekuwa changamoto kubwa sana kwa wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro. Je, ni lini wananchi wa Wilaya ya Ngorongoro watapata umeme wa uhakika?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kujibu swali la Mheshimiwa Festo, maeneo yote ambayo yana changamoto ya umeme kufika katika maeneo yale kwa sababu ya kusafirishwa kwa umbali mrefu yamechukuliwa katika Mradi wetu wa Gridi Imara. Nimhakikishie Mheshimiwa Catherine Magige nitawasiliana naye kumwonesha plan ya Serikali ya kuhakikisha Wilaya yetu ya Ngorongoro inapata umeme wa uhakika na unaotoka katika maeneo yake kwa sababu, kuna wananchi ambao wanatakiwa pia wapate huduma hiyo kwa usahihi kabisa.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Pamoja na maelezo mazuri ya Serikali nina swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kweli anasema kuna mitandao ambayo inatumika kuhudumiwa na TANESCO lakini Kibiti ni moja ya mkoa ambao uko Kusini mwa Mkoa wa Pwani ambapo kuna mikoa minne; Mkuranga, Mafia pamoja na Rufiji. Sasa hatuoni umuhimu wa kujenga kituo kikubwa sana kwa sababu hapo ni centre ya mikoa ya Kusini ya Mkoa wa Pwani, kituo kikubwa ambacho wananchi wataweza kufika sababu sio vijiji vyote ambavyo wanaweza kufikiwa na mambo ya mtandao? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, kama nilivyoeleza kwenye jibu la msingi, tunaendelea kufanya tathmini kwenye paragraph ya kwanza. Nimesema kwa umahususi wa Kibiti kwa ajili ya kuona namna ambavyo tutafanya ili kujenga ofisi hii ili iweze kuhudumia maeneo ya Kibiti lakini na maeneo mengine ya Jirani.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante, Miji wa Iringa ni kivutio cha utalii Kusini na katikati ya mji tumeboresha sana majengo yetu. Kuna jengo la TANESCO la Ofisi ya Mkoa ambalo limetelekezwa muda mrefu, ni lini mtalimalizia ili liendelee nalo kuchangia uvutiaji wa Kusini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Katika maeneo yote ambayo majengo hayajakamilika ni swala la kibajeti na tunaendelea kujikusanya kwenye fedha na kutanguliza vipaumbele lakini nimhakikishie Mheshimiwa Jesca kwamba jengo hilo pia litakamilishwa ili liweze kuwahudumia wananchi lakini kama ulivyosema liwe kivutio cha utalii Iringa.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Wilaya ya Kahama ina Halmashauri tatu na hivyo kusababisha changamoto ya kupata huduma kwa wakati. Lini sasa Serikali inampango wa kuanzisha Mkoa wa ki-TANESCO katika wilaya ya Kahama ili isaidie kutoa huduma kwenye maeneo yale? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kweli Wilaya ya Kahama inazo Halmashauri tatu na sisi tunayo Ofisi ya Kiwilaya ya TANESCO kama zilivyokuwa ofisi nyingine za Serikali na tunachokifanya ni kuendelea kupeleka huduma kwa wananchi kwa kufungua ofisi ndogo au viunga kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, jambo la kufungua Ofisi ya Kimkoa ya Ki-TANESCO tunaendelea kulitizama kwa sababu zinazo viwango na grade mbalimbali na zitakapokuwa zimekamilika tutakamilisha jambo hilo kwa ajili ya huduma kwa wananchi.
MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Katika mpango huo vipo vijiji vinne ambavyo havikuwekwa kwenye mpango, sijui sababu ni nini. Vijiji hivyo ni Kelemakuu, Birise, Muungano na Sankaleti. Nataka kujua, Serikali ina mpango gani sasa wa kuviingiza vijiji hivyo kwenye mpango wa REA? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Monni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba vijiji hivyo vinne vya Kilemakuu pamoja na vingine vyote vipo katika hivyo vijiji 12 ambavyo vimebakia katika utekelezaji wa mradi na kufikia hiyo tarehe 31 Oktoba vitakuwa pia vimewashiwa umeme. (Makofi)
MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Usimikaji wa nguzo katika Kata ya Likawage na Vijiji vyake vya Nainoku, Liwiti na Likawage yenyewe katika Jimbo la Kilwa Kusini umekwama kutokana na changamoto ya TFS kuzuia kupitisha nguzo katika eneo la hifadhi. Je, ni nini mpango wa Serikali wa kushirikiana kati ya Wizara ya Nishati na Wizara ya Maliasili na Utalii kuondoa utata huu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kassinge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli, awali kulikuwa kuna changamoto kubwa ya Sheria ya TFS ambayo ilikuwa inatutaka sisi Wizara ya Nishati au watumiaji wengine wa maeneo yao kulipia gharama fulani lakini baada ya majadiliano tumekubaliana kwamba, kwa sababu tunafanya miradi ya Serikali kwa pamoja basi tupeane hizi leeway kwa ajili ya kupitisha hii miundombinu. Kwa hiyo, case by case zikitokea tunazi-solve kulingana na maeneo husika. Nitawasiliana na Mheshimiwa Mbunge ili tuone wapi tulipokwama na tuweze kutatua tatizo hili kwa sababu maeneo mengine tayari tumelimaliza.

MHE. HAWA S. MWAIFUNGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Kumekuwa na changamoto kubwa ya kurukwarukwa kwa kuwekewa umeme kwa wananchi katika Kata za Kalunde na Ndevelwa katika Jimbo la Tabora Mjini. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawekea wananchi wote umeme kwa usawa ili waweze kunufaika na huduma hii? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Hawa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba hatujaweza kama Serikali kuwa na uwezo wa kumuunganishia kila mwananchi anayehitaji umeme leo, lakini mpango mkubwa wa Serikali ni kutafuta shilingi takribani trilioni sita na bilioni kama mia tano ambazo zitafikisha umeme kila kitongoji katika nchi hii, kila mtaa katika nchi hii. Hivyo, tunaamini wananchi walio wengi kwenye maeneo hayo wataweza kuupata umeme kwa wakati mmoja. Kwa sasa, kwenye mradi tuliokuwa nao wa REA III round II, tunaenda na wananchi wachache kama sampling kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mradi umeanza, lakini tunaendelea kuongeza kuwafikia wananchi wengine kwa kadri ya uongezekaji wa bajeti.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Wananchi wa Kijiji cha Nyabikurungo Kata ya Ukuraijo waliwekewa nguzo na baadaye zikaondolewa bila kuunganishiwa umeme lakini pia Kijiji cha Bugaza, Kata ya Kimuli. Nataka kujua ni lini hawa wananchi watawashiwa umeme katika hayo maeneo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba programu yetu ya kupeleka umeme vijijini itakamilika mwezi Disemba mwaka huu. Namhakikishia Mheshimiwa Mbunge kwamba kijiji hicho pia kitapata hiyo nishati ya umeme na mkandarasi anayepeleka umeme wa Rukomi na Kawahya tutamsimamia ili aweze kufanya kazi hiyo kwenye maeneo hayo.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, tuna vijiji zaidi ya hivyo ambavyo amevitaja Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa mfano vijiji vya Gundusini, Mabilioni, Gavao, Saweni, Rwinndini, Ruvu, Jiungeni, Mferejini, Duma, Emugule na Endevesi vyote hivi havina umeme. Sasa Mheshimiwa Waziri atakuwa tayari tutembelee vijiji hivi ili aone hali halisi kuliko kwamba zinawekwa nyumba mbili halafu tunaambiwa Kijiji kimewekewa umeme? Hilo halitakubalika.

Mheshimiwa Spika, la pili. Je, Serikali iko tayari kutoa kwa Wabunge orodha ya Wakandarasi wale wanaokwenda kuweka umeme katika maeneo yao ili nao waweze kufuatilia? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru Waheshimiwa Wabunge jana wametupitishia bajeti kwa ajili ya kwenda kutekeleza miradi na ahadi ambazo tumezitoa. Pia nimwahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba niko tayari kuambatana naye kwenda jimboni kwake baada ya Bunge kuisha ili kuona vijiji hivyo ambavyo havijafikiwa na umeme. Kama tulivyosema viko tisa na ni kweli hata jana tumesoma kwenye bajeti, tunatambua kwamba sio wananchi wote na vitongoji vyote vimepata umeme, lakini jitihada na hatua zimeanza na tunaamini tutakamilisha. Ifikapo Desemba, 2023 hatutarajii kuwa na kijiji ambacho hakijafikiwa na miundombinu ya umeme.

Mheshimiwa Spika, katika eneo lingine, tuko tayari na tulishafanya hivyo na tutafanya tena kuhakikisha kila Mbunge anamfahamu Mkandarasi wake na scope yake na wale wanaosaidia katika usimamizi. Nikitoka hapa nitapitia kwa Mheshimiwa Mbunge nimpatie pia wale wa kwake wanaofanya kazi kwenye maeneo yake ili aweze kuwa na nafasi nzuri ya kufanya ufuatiliaji yeye mwenyewe.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, naomba niishukuru sana Serikali kwa majibu mazuri, lakini bado kasi ya utekelezaji wa miradi inakwenda taratibu sana. Swali la kwanza: Je, Mheshimiwa Waziri, uko tayari kuambatana nami ili twende jimboni ili tukasukume kwa pamoja utekelezaji wa miradi hii katika jimbo langu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Kata ya Bunambiyu pamoja na Mwasubi ni maeneo ambayo zikinyesha mvua huwa hayapitiki ni maeneo ambayo yanapata maji kwa wingi sana. Sasa, mko tayari kuhakikisha kwamba mnaweka msukumo mkubwa ili maeneo hayo yapewe kipaumbele, wakati huo huo maeneo hayo niliyoyataja na yenyewe yaweze kufanyiwa kazi kwa haraka?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza nampongeza Mheshimiwa Boniphace, amekuwa akifuatilia sana haya maeneo na mradi ule mkubwa wa umeme wa kutumia solar ambao tumeufanikisha juzi kuusaini, na katika Jimbo lake, mkoa wote wa Shinyanga na nchi nzima itakuwa ni faraja kubwa.

Mheshimiwa Spika, namuahidi kwamba niko tayari kuambatana naye kwenda kuhakikisha tunaendelea kumsimamia mkandarasi huyu kama tulivyoahidi katika bajeti. Vile vile, mbinu za kufungua LC, kuongeza wasimamizi na kuwawezesha, zitatusaidia kuhakikisha kwamba ndani ya muda tunakamilisha kazi hii. Hilo jambo la maeneo ambayo yana changamoto, tutalichukua kwa ukubwa wake ili kuhakikisha tunamaliza kazi hii mapema kwa mujibu wa mkataba. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Mimi ni Mbunge wa Tarime Vijijini, pale Nyamwata, Kerende, Nyangoto ni vijijini kabisa. Maeneo haya yote wananchi wanalipa umeme kwa gharama kubwa. Kwa hiyo, Jimbo limegawanywa kuna watu wanalipia umeme kwa bei ya chini ya shilingi 27,000 na wengine bei kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nijue ni lini mchakato huu wa kurudisha bei ya shilingi 27,000 ya umeme kwa watu wa vijijini inarudishwa ili watu wapate umeme sawa? Huu mchahakto umechukua muda mrefu.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwikwabe Waitara, kwamba ni kweli tumebaini yapo maeneo mengi ambapo tulipofanya tathmini awali tumeyaacha, wale wataalam wameelekezwa warudi tena ili wakifanya iwe ni once and for all. Kwa hiyo, wanapita kwenye maeneo yetu, kazi ni kubwa inahitaji weledi na utulivu mkubwa ili tuweze kuwahudumia wananchi vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waitara na Waheshimiwa Wabunge mtuvumilie kidogo tulikamilihse hili kwa usahihi na ufasaha kabisa. Tutakapokuja kuleta mbele yenu liwe ni tatizo ambalo tumelikamilishwa tuende kwenye hatua nyingine. (Makofi)

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa na sintofahamu sana kwa wananchi wengi wakiwepo wa Jimbo la Kibamba kubambikiwa madeni makubwa ya ununuzi wa umeme au LUKU bila kuelewa kutokana na kukosewa kwa makadirio ya awali na TRA. Je, Serikali mko tayari kuwaelekeza TRA waweke mpango mzuri ambao wananchi hawa wataweza kupunguza madeni yale kila mwezi wakiwa wanalipa LUKU zao kila mwezi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Mtemvu, kwa swali lake. Juzi wakati tunapitisha bajeti jambo hili lilijitokeza na ulitolewa Mwongozo na Mheshimiwa Spika kwamba, Wizara ya Nishati pamoja na wenzetu TRA ambao hasa ndiyo wenye hizo pesa tukae na kuweka utaratibu mzuri. Sisi tumeshawafikishia wenzetu, tumewapelekea concern hiyo wanatengeza utaratibu mzuri wa kuonesha deni na mwananchi aweze kulipa taratibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hili Wizara ya Nishati kupitia TANESCO ni kama bomba la kupitisha mapato hayo ambayo yanatoka kwa mwananchi kupitia TRA. Hata hivyo, tunashirikiana na wenzetu kuweka mifumo mizuri ili wananchi wanaopata huduma ya umeme sasa wasipate adha ya kulipa kodi hii ya majengo ambayo inapitia kwetu. Kwa hiyo, tutalifanyia kazi kwa pamoja Serikalini.
MHE. DEO K. SANGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali ambayo Wizara hii ndiyo Wizara pekee iliyotengewa bajeti ya zaidi ya shilingi trilioni tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa majibu ya Serikali ni mazuri vipo baadhi ya Vijiji – Miji vinavyofanana na hivi alivyovitaja ikiwemo Ibumila na maeneo mengine. Je, Serikali iko tayari sasa kuwapatia wananchi umeme kwa bei ya vijiji kama alivyotaja vikiwepo Vikwete, Mkolango na Malombwe?

Swali la pili, kwa kuwa wananchi wa Makambako wa Kata ya Kivavi na Kata ya Majengo wameathirika kwa muda mrefu wakisubiri umeme wa upepe na kulipwa fidia zaidi ya miaka 20. Je, Serikali inawapa majibu gani wananchi hawa ili kama haiwezekani wananchi waendelee na shughuli zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la kwanza la swali la Mheshimiwa Sanga, Serikali inayo nia ya dhati kabisa kuhakikisha kwamba wananchi wanaunganishiwa umeme kwa gharama nafuu ambazo wanazimudu. Kama tulivyosema juzi kwenye bajeti yetu, tunaendelea kufanya tathmini na upembuzi yakinifu kubaini ni maeneo gani yanaweza yakawa yanakidhi gharama hizo za shilingi 27,000 pia kutafuta chanzo kizuri na cha uhakika cha kuweka ruzuku katika eneo hilo, kwa sababu ni kweli gharama za kuunganisha umeme ni kubwa. Pale ambapo tunatakiwa kuunganisha kwa shilingi 27,000 basi inabidi kuwekwa ruzuku kubwa na tunapounganisha kwa 320,000 basi tunaweka ruzuku kama nusu. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Sanga na wengine wote kwamba jambo hili Serikali imeshalichukua na inalifanyia kazi tunaamini litakamilika siku chache zijazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye eneo la pili, ni kweli kwamba wananchi wa maeneo ya Makambako wameahidiwa kupewa umeme wa kutumia upepo na maeneo yao yalainishwa kwamba yatalipiwa fidia kwa muda mrefu. Tumechukua muda mrefu kwenye mazungumzo na wale waliotaka kuwekeza ninapenda kusema kwamba tumefikia hatua ya mwisho ya mazungumzo hayo, ambapo TANESCO tayari wamekwishatengeneza mkataba wa makubaliano na wanaupitisha kwenye taasisi yao na baadae utakuja Wizarani ili utolewe sasa kwa ajili ya kuendelea na hatua nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wananchi wa Makambako kabla ya mwezi wa Tisa shughuli zitaanza site kwa kulipa fidia na kuanza kutekeleza mradi utakaotuongezea umeme wa upepo kwenye gridi yetu ya Taifa.(Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mji wa Liwale unaoundwa na Kata tatu, Kata ya Likongole, Liwale Mjini na Nangando vipo vijiji zaidi ya kumi lakini vijiji vile vimegawanya, kuna vijiji vinalipa shilingi 27000 na kuna vinavyotakiwa kulipa shilingi 350,000. Je, Serikali haioni kwamba kwa sababu vyote hivi ni vijiji viingizwe kwenye kulipa shilingi 27000 ili kuweka usawa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nifafanue kidogo jibu ni lilelile lakini niliongezee nyama kidogo.

Mheshimiwa wenyekiti, Wizara ya Nishati kupitia TANESCO tulibaini maeneo ya Vijiji na Miji kutoka kwenye taarifa za wenzetu wa TAMISEMI ndiyo waliotupatia taarifa za hapa ni mjini na hapa ni kijijini. Baada ya ku– implement hicho tulichokipata ndiyo yakatokea maoni mbalimbali kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge na wananchi. Tukaona ni vema tuende site wenyewe ili tukabaini, pamoja na kwamba enzetu wa TAMISEMI wamesema hapa ni mjini lakini maisha ya pale yanaonesha kuwa ni kijijini na hilo ndilo zoezi tunalolifanya na tukilikamilisha tutashirikiana na wenzetu wa TAMISEMI ili kuweka usawa kama ulivyoshauri Mheshimiwa Kuchauka ili wananchi waweze kulipa ile gharama ambayo wanaweza kuilipa kutokana na mapenzi na utashi mwema wa Serikali kuhakikisha kwamba inawahudumia wananchi wake salama.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Mimi nina swali moja.

Je, Serikali hamuoni umuhimu wa kumaliza utengenezaji wa umeme katika Jimbo la Temeke hasa Jimbo la Mjini, ukizingatia kuna wakati umeme unakatika kwenye viwanja hasa katika mechi hizi za Kimataifa, ni lini sasa mtarekebisha umeme huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la Mheshimiwa Dorothy Kilave ni la msingi kabisa. Tunayo nia ya dhati kama Serikali kumaliza tatizo la kukatika umeme Tanzania nzima. Tunashukuru kwamba juzi mmepitisha bajeti ya Wizara ya Nishati yenye fedha za kutosha kwa ajili ya kuhakikisha tunaondokana na tatizo hili. Tuwahakikishie litakwisha kupitia mradi wetu wa gridi imara tutaendelea kuimarisha maeneo mengi ambayo yana changamoto kubwa ya ukatikaji wa umeme ikiwemo Jimbo la Temeke. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kumekuwepo na kukatwa kwa kodi za majengo kwa wale ambao hawastahilin kukwatwa kwa mfano, wazee na zile nyumba za tembe. Sasa, ninataka kujua ni lini Serikali itafanya reconciliation ili iweze kuwarudishia gharama zote ambazo wamekatwa hawa ambao hawastahili kukatwa kodi hizi za majengo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema na kama tulivyosema kwenye budget speech ya juzi, wenzetu wa Wizara ya Fedha wameshalichukua nasi tulichowa-supply ni namba za LUKU kwa ajili ya wao kuwa-identified nani anastahili kulipa kiasi gani na kwa wakati gani na kwa utaratibu gani. Tunashirikiana nao wenzetu ili waweze kuweka utaratibu mzuri ambao utahakikisha yule anayetakiwa kulipa kweli ndiye anayelipa kama tulivyosema juzi kiwanja kimoja kinaweza kuwa kina vyumba vitano, sita halafu kila mmoja analipa wakati hakutakiwa kulipa kilo mmoja, lakini tunafahamu pia sheria nyingi zinaeleza kwamba wale wazee wa miaka 60 na zaidi wawe-exempted kwenye hayo maeneo na wastaafu wengine tumeshawasiliana na wenzetu na tunalifanyia kazi naamini wenzetu wa Wizara ya Fedha watakamilisha na tutafikia sehemu nzuri.

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kama ilivyo Mkoa wa Songwe pia katika Mkoa wa Mtwara kuna vijiji 102 bado havijapatiwa umeme. Nataka kujua Serikali ni lini itavipatia vijiji hivyo umeme?
Swali la pili, kwa kuwa umesema mnafanya mchakato wa kutambua Kata ambazo zina hadhi ya Miji lakini ni Vijiji. Nataka kujua ni lini mchakato huo utakamilika ili watu wapate huduma kwa sababu hata katika Jimbo la Mtwara Mjini kuna baadhi ya Kata mfano Kata ya Naliendele, Kata ya Jangwani na zingine zinaonekana ziko Mjini lakini maisha ya watu wake ni kama wako vijijini, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tunza Malapo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, alivyosema kama ilivyosomwa lakini na Mtwara pia tunao Wakandarasi wawili, wanafanya kazi katika Mkoa wetu wa Mtwara na juzi tulikaa kikao na Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara tukajadiliana kwa upana namna ya kumaliza haraka kazi hizo, tunaamini kwa mkakati tuliouweka kabla ya Desemba mwaka huu kazi yetu ya kupeleka umeme katika vijiji vyote vya Mkoa wa Mtwara itakuwa imekamilika na hilo tunauhakika nalo na tunawahakikishia Waheshimiwa Wabunge kwa kutupitishia bajeti juzi tutaendelea kusimamiana na wenzetu ili kazi hii iweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili ni lini tutamaliza kazi hii, tunatamani hata tuimalize leo lakini kwa sababu ya kutaka kufanya ushirikishwaji mkubwa na kubaini changamoto za maeneo mbalimbali tunaomba mtuongezee muda kidogo halafu baadae tutakuja kusema ni lini tutamaliza ili tuweze kukamilisha hii kazi kwa Pamoja, tusingependa kuikimbiza harafu ikawa kama ya awali ambayo haikuleta majibu tuliyokuwa tunayatarajia kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naishukuru Serikali kwa kuwa tayari Mkandarasi wa REA katika Halmashauri ya Mji wa Mbulu ameshasimika nguzo kwenye vijiji vyote yapata miezi minne. Je, ni lini sasa wananchi wale wa Vijiji vya Mbulu Mjini watapewa umeme kwa kuunganishiwa nyaya na kuunganishiwa umeme kwenye makazi yao?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema miradi yote ya REA three round two itakamilika kufikia Desemba mwaka 2023 lakini kwa nyakati tofauti tofauti vijiji mbalimbali vitaendelea kuwashiwa umeme. Kama alivyosema Mheshimiwa Issaay hayo maeneo ambayo tayari wameshasimika nguzo tunatarajia kwenye mwezi mmoja mpaka miwili tayari kazi itakamilika wakati maeneo mengine tunaendelea kuchimba, kusimika nguzo na kuunganisha umeme, lakini ifikapo Desemba kazi yote itakuwa imekamilika.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Vijiji 33 vya Bunda vilipewa umeme kilomita tatu kwa kila kijiji na sasa Mkandarasi amepeleka kilomita moja kwa kila kijiji. Ni lini kilometa mbili zitaongzwa katika vijiji 33 vya Jimbo la Bunda?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Getere kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Wabunge wa Mkoa wa Mara kwamba katika zile lot ambazo Wakandarasi wao tayari wamekamilisha original scope kwa asilimia 100 na Mkandarasi wa Mkoa wa Mara tayari naye yumo katika orodha ile, kwa hiyo tuendelee kusukuma kwa pamoja ili tuweze kukamilisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunatarajia mwishoni mwa wiki hii wanzetu wa REA watasaini mikataba na wale ambao wamepata nafasi ya kuongeza hizo kilomita mbili ambazo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ametoa bilioni 351 kwa ajili ya kuongeza kilomita mbili kwa kila Kijiji. Tunatarajia wiki hii zitasainiwa na hivyo mwanzoni mwa mwezi unaokuja kazi za kusimika nguzo na kuvuta waya utaanza katika maeneo hayo ambayo nyongeza ya kilomita mbili inaenda kufanyika.
MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Swali langu ni dogo. Je ni lini mradi wa kilomita mbili za nyongeza katika mradi wa REA III round two utaanza kutekelezwa katika Mkoa mzima wa Mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema kwa Mheshimiwa Getere nipende kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Masaburi kwamba tunatarajia Ijumaa ya wiki hii wenzetu wa REA watakaa na wakandarasi. Tayari wameshapewa idhini ya kuendelea na maeneo hayo ya kutekeleza kilomita mbili na wakishasaini mikataba mwishoni mwa wiki hii tunatarajia mwanzoni mwa mwezi unaokuja kazi itaanza na kwa kuwa ni kazi ndogo tunatarajia itakamilika pamoja na kazi kubwa mwezi Desemba mwaka huu kwa sababu ni kupeleka line ndogo za kuwasha umeme katika vijiji vyote ambavyo vilikuwa katika REA III round two kwa maana ya kuongeza kilomita mbili kwa kila kitongoji. Nakushukuru.
MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nami naomba niulize swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kijiji cha Majengo, ramani ya umeme imepeleka umeme kwenye kitongoji cha Nshepa badala ya makao makuu ya Kijiji. Je Serikali iko tayari kutoa maelekezo katika vile vitongoji 15, makao makuu ya Kijiji cha Majengo yapelekewe umeme mwaka huu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kakunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, vitongoji 15 ambavyo tumepata pesa jumla ya shilingi bilioni 357 kwa ajili ya kuongeza vitongoji 15 kwa kila Jimbo, tulisema juzi katika bajeti na nirudie tena, litakuwa ni chaguo la Mheshimiwa Mbunge mwenyewe kuchagua ni wapi hivyo vitongoji 15 apelekewe. Kwa sababu kama anavosema Mheshimiwa Aweso kwamba anayelala na mgonjwa ndiye anajua mihemo yake, tunaamini Waheshimiwa Wabunge mnatambua zaidi mahitaji yako wapi kutuzidi sisi. Kwa hiyo, tuyashirikishana pamoja na ninyi kujua na kutambua ni maeneo gani ya vitongoji viwe vya kipaumbele wakati tukiwa tunaelekea kupata pesa nyingi ili kumaliza vile vitongoji 36,101 ambavyo bado havijapatiwa umeme. (Makofi)
MHE. EMMANUEL A. MWAKASAKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi nami kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye miradi mingi ya REA katika baadhi ya vijiji hawa Wakandarasi wamekuwa hawawalipi vibarua na kuna malalamiko mengi. Serikali inachukua hatua gani kuhakikisha hawa Wakandarasi wanawalipa wale vibarua ambao wanafanya kazi hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kama anavyosema Mheshimiwa Mwakasaka, tumekuwa na changamoto hiyo ya Wakandarasi ama kuchelewa sana au kutolipa kabisa malipo ya vibarua wanaofanya nao kazi. Tumelichukulia hatua kwa kuwa tunawasiliana na wale watumishi wa hao Wakandarasi na kuwashauri wanapokuwa wanaingia katika engagement hizi watengeneze vikundi na wawasiliane na Ofisi zetu za Serikali zilizopo kwenye maeneo husika ili changamoto inapotokea tuibaini mapema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Mkoa wa Tabora tumeendelea kushughulikia matatizo hayo nasi ofisini tumeshapata watu mara kadhaa ambao wamekuja na tumewapeleka REA pesa yao imeweza kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaahidi Waheshimiwa Wabunge kwenye maeneo yetu yote wale wote wanaofanya kazi ujira wao halali utalipwa kwa sababu Serikali inamlipa Mkandarasi na Mkandarasi lazima alipe kwa wale vibarua ambao amefanya nao kazi. (Makofi)
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza kwa vile taarifa za TAMISEMI hazikuwa sahihi je, Serikali iko tayari kuwarejeshea wananchi pesa ambazo zimezidi kutoka shilingi 27,000 hadi 321,000 baada ya taarifa yetu kujulikana kwamba siyo sahihi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, je, zoezi la kubaini vijiji mji ambavyo vimetajwa hapa kwenye swali la msingi litakamilika lini ili wananchi wenye uwezo mdogo kwenye vijiji vyetu waweze kupata umeme ikiwemo Kaduda, Chibingo, Ibondo na vingine vingi? Naomba kuwasilisha.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali ya nyongeza mawili ya Mheshimiwa Tumaini Mbunge wa Busanda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba niweke taarifa sahihi kwamba tunaamini kabisa taarifa za TAMISEMI zilikuwa sawa kwa mujibu wa Sheria ya Mipango Miji. Isipokuwa kinachogomba ni ile hali ya kwamba watu wanatambuliwa kuwa wako mjini lakini wao wanajiona hawako Mjini na kwa sababu tumelibaini hilo tumeona ni vema sasa sisi Wizara ya Nishati twende site na kubaini hata kama eneo ni la mji, lakini je, uhalisia wa maisha ya wakazi wa maeneo yale ni wa namna gani? kwa sababu Sheria ya Mipango Miji imeweka maeneo na mazingira ya masharti kama kuna maduka, kama kuna vituo vya afya, kama kuna barabara za lami na nini hayo ndiyo maeneo ya mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme tu taarifa ya TAMISEMI kwa mujibu wa sheria ilikuwa sawa. Lakini maeneo hayo yanawakazi wenye vipato tofauti na hivyo sisi tunafanya utafiti na upembuzi yakinifu kuona ni kiasi gani kilipwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo hapo niseme kwamba anaposema turudishwe kwa wananchi namuomba asielekee huko. Kwa sababu Serikali ya Awamu ya Sita inaweka ruzuku kwenye gharama za kuunganisha umeme kwa kulingana na maeneo mbalimbali yalivyo. Kwa hiyo Serikali iliweka ruzuku hata hii 320,000 bado ni ruzuku imewekwa ili wananchi waweze kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa shughuli ikikamilika ambayo ameuliza kwenye eneo la pili ni lini? Tunaendele, tunafanya kazi hii ni kubwa tulimaliza awamu ya kwanza tukaona kuna maeneo hatukufika tumerudi. Tunaomba yeye na Waheshimiwa Wabunge wawe wavumilivu ili zoezi litakapokamilika tuweze kuja kutoa taarifa sahihi na kuweza kutangaza gharama sahihi kila eneo.
MHE. KENNETH E. NOLLO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Nataka tu nijue Serikali inatumia kigezo gani? tofauti ya 27,000 na shilingi 300,000 ni kubwa mno je, Serikali haioni hebu ije na mkakati wa kuona kiwango fulani ambacho kitakuwa kina rationale nzuri kwa wote wanaokaa mjini na wale wa vijijini? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma kuliwahi kuwa na viwango tofauti tofauti vya kuunganisha umeme. Sasa kwa maneno machache niseme tulipata kipindi fulani mradi wa kupeleka umeme vijijini na ulikuwa unafanyika bure kwa watanzania wote waliyokuwa wanakidhi vigezo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ule mradi ulikuwa wa mfadhili na mfadhili akasema hawezi kutoa bure, kwa hiyo, tutakubaliana kwamba basi mwananchi alipie VAT ambayo kipindi hicho VAT ilikuwa ni shilingi 27,000 ndiyo genesis ya shilingi 27,000 ilipoanzia. Kwa hiyo, tumekwenda nayo kwa utaratibu huo mpaka sasa na Serikali sasa ndiyo inafanya mchakato na upembuzi mpana zaidi ili kuona kama tunaweza tukawa tuna viwango tofauti tofauti kwa misingi tofauti tofauti kama hii 27,000 ilikotokea kipindi hicho ilikuwa kuunganisha, ilikuwa 150,000 nadhani sasa asilimia 18 au 20 nadhani VAT ilikuwa asilimia 20 ikawa ni shilingi 27,000 ndiyo genesis ya shilingi 27,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama halisi ni shilingi laki saba, laki sita mpaka laki saba. Kwa hiyo, inapungua kwenda laki tatu kulingana na ruzuku ambayo inayotolewa na Serikali kwenye maeneo ya mijini na maeneo ya vijijini au kwenda shilingi 27,000. Nashukuru.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru Kijiji cha Luganga na Kijiji cha Kilolo ndipo yalipo Makao Makuu ya Wilaya lakini hivi ni vijiji vilivyosajili. Je, Serikali ipo pia tayari kuangalia hivi vijiji kwa sababu wamepewa kulipa zaidi ya shilingi 300,000 ambayo ni tofauti na 27,000 kwenye vijiji vingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuhakikishie Mheshimiwa Nyamoga kwamba maeneo yote yatafikiwa na upembuzi huu unafanyika nchi nzima kwenye maeneo yote ili kuweza kubaini uhalisia wa kila eneo.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama navyofahamu wafugaji hawaishi mjini sasa vijiji vya Kisimani na Kilimani pale Himo viliingizwa kwenye Mji mdogo wa Himo na hivyo kukosa fursa ya kufurahia umeme wa REA. Je, mnatoa kauli gani kuhusu hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Kimei kwamba azma na nia ya Serikali ya Awamu ya Sita ni kuhakikisha kila Mtanzania popote alipo anapelekewa huduma ya umeme na tayari tumeshaanza kufikisha kwa kila kijiji. Lakini hatua kubwa inayofuata ni ya kupeleka kwenye vitongoji ambavyo hata juzi kwenye bajeti tumevisema na tunatarajia pesa kubwa tutaipata kwenye mwaka wa fedha ule mwingine unaofuata ili vitongoji vyote maana yake wananchi wote waweze kupata huduma ya umeme popote walipo.

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Jambo la kwanza kwa niaba ya wananchi wa Makete tuishukuru Serikali kwa mradi huu ambao ni mradi mkubwa ambao tayari dermacation imeshafinyaka na sisi wananchi wa Makete tupo tayari kupokea. Utayari wa Serikali kwamba Mwezi wa saba itaanza kulipa fidia kwa wananchi wetu kwa mwaka huu. Maswali yangu mawili ya nyongeza ni yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaozunguka eneo hili la bwawa wa Vijiji vya Busokelo, Madihani, Bulongwa, Mwakavuta, Itete pamoja na Ruangwa; vijiji hivi vyote sasa hivi shughuli za kiuchumi zimesimama kwa sababu ya dermacation. Sasa tulikua tunaomba kujua;

Je, mko tayari kuturuhusu wananchi waweze kulima yale mazao ambayo yanaweza kuondoka wa mfupi kwa maana ya mahindi, njegere na shughuli zingine ambazo hazichukui muda mrefu, kwa sababu muda huu shughuli zote zimesimama?

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, bwawa hili linahusisha miradi ya ujenzi wa barabara, kwa maana ya kutoka Makete kuelekea Busokelo kwa Mheshimiwa Mwakibete;

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha miundombinu hii inajengwa kwa sababu huu ni mradi mkubwa ambao utapitisha vifaa vingi; Serikali itajenga barabara hizi lini wakati wa utekelezaji wa mradi huo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa niaba ya Serikali na mimi nipokee shukurani na pongezi za Wananchi wa Mkoa wa Njombe kwa ujumla na Mkoa wa Mbeya ambako bwawa linafika hadi Busokelo. Lakini nimuombe Mheshimiwa Sanga aendelee kuwashawishi wananchi watuvumilie kwa sababu tunatarijia kuanza kulipa fidia mwezi unaokuja au labda mwezi unaofuata baada ya hapo. Katika muda mfupi wananchi watapata kile ambacho wanakistahili ili eneo hili waliweze kuliacha kwa ajili ya sasa Serikali kuwa tayari kufanya shughuli zake ambazo ni za uendelezaji wa mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimuahidi Mheshimiwa Sanga kwamba wananchi hawatachukua muda mrefu watakuwa wamepata fidia yao na wanaweza wakaendelea kujiendeleza kwenye maeneo yao na maeneo yao. Lakini pembeni ya hilo tutaendelea kujadiliana na tuzungumze. Tunayo experience mbaya, kwamba tunapotoa nafasi kama hiyo wananchi sasa wanarudi moja kwa moja hata baada ya kulipwa fidia wanataka waendelee kubaki kwenye maeneo yao. Kwa hiyo, tutajadiliana na viongozi wa Serikali wa maeneo husika na wewe Mheshimiwa Mbunge ili tuone namna bora ya kuwahudumia wananchi katika kipindi hiki ambacho ni cha mpito

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kwenye eneo la pili, ni kweli tutagenga miundombinu mbalimbali katika maeneo hayo barabara, madaraja kwa ajili ya kubeba mzigo kuhudumia mradi. Na kwa sababu mradi bado haujaanza, plan yetu ni kuanza kulipa fidia tukamilishe mambo madogo madogo halafu tujenge miundombinu kwa ajili ya kuweze kufikia lile eneo. Kwa hiyo kabla ya mradi kuanza mwaka wa fedha ule mwingine unaokuja barabara na maeneo mengine yanayotakiwa kuwekea miundombinu itawekwa ili ihudumie eneo la mradi lakini pia ihudumie wananchi kwa maendeleo yao ya kila siku.
MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona.

Je, ni lini Wananchi wa Kitongoji cha Cheketu, Kijiji cha Somanga Kusini, Wilayani Kilwa watalipwa fidia ya kupisha ujenzi wa miundombinu ya umeme katika eneo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la Mheshimiwa Ndulane linahusiana na ujenzi wa mradi wa kujenga kituo cha kuzalisha umeme kwa kutumia gesi Megawatt 350 pale Somanga Fungu, na tayari tumepata mfadhili, mwenzetu wa JICA, tunaendelea na kukamilisha mazungumzo. Tutakapokuwa tayari kumaliza mazungumzo na kujenga mradi wananchi wa eneo hilo watapewa fidia yao. Tuombe Mheshimiwa Mbunge aendelee kutusaidia eneo hilo liendelee kulindwa ili muda wa kulipa fidia utakapofika basi isiwe ni shida kulipa fidia.
MHE. CATHERINE V. MAGIGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Katika Mkoa wa Arusha maeneo mengi hususan Wilaya ya Monduli umeme wa REA nguzo zimesimikwa nyanyazimeshawekwa lakini mpaka leo wananchi hawajapata umeme;

Je, ni lini sasa wananchi hawa watapata umeme ili waondokane na adha hii kubwa ya kukosa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna maeneo mengi ambapo nguzo zimesimikwa na miradi haijakamilika. Katika maeneo aliyoyataja ya Monduli na maeneo mengine Arusha tunaye mkandarasi anayeitwa ambaye tayari yuko kazini anaendelea na kazi. Nimuahidi Mheshimiwa Mbunge Catherine Magige pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote kwamba kabla ya Desemba mwaka huu miradi yote ya REA III Round II itakuwa imekamilika na ndugu zetu wananchi wa Monduli na wengine watapata umeme kwa kadri tulivyokubaliana.
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nataka nijue ni lini sasa REA Phase Three Round Two ya kusambaza kilometa mbili za ziada kwenye Wilaya ya Rorya utaanza kufanya kazi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali langu la pili. Kampuni tanzu ya ETDCo imepewa kazi zaidi ya miaka mitatu sasa kusambaza umeme wilaya ya Rorya, lakini mpaka sasa hawajaanza kufanya kazi.

Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kumfuta mkandarasi huyu ili itangaze upya waombe wakandarasi wengine kwa ajili ya kusambaza umeme Wilaya ya Rorya?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, leo tunatarajia wenzetu wa REA watasaini baadhi ya mikataba ya extension ya kilomita mbili kwa kila kitongoji na tunaamini kufikia mwishoni mwa mwezi huu wakandarasi hao watafika site ili kuanza kufanya kazi hizo za kuongeza hizo kilometa mbili kwenye maeneo ambayo mikataba ya vijiji imekamilika na pengine inaendelea.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, naomba baada ya hapa nikae na Mheshimiwa Chege ili tuone tatizo liko wapi kwa sababu tunafahamu miradi mingi inaendelea kwa hatua mbalimbali katika maeneo yetu, specifically nitakaa ili tubaini changamoto aliyoiona iko wapi na tuweze kueleweshana na kuchukua hatua stahiki.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kunipa nafai hii.

Je, Serikali itamaliza lini ujenzi wa kituo cha kupozea umeme kinachojengwa katika Kijiji cha Uhuru, wilayani Urambo ili kumaliza tatizo la umeme tulilonalo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mradi wa kujenga kituo cha kupoza umeme cha Uhuru kilichoko Urambo ni mojawapo ya miradi yetu 14 ya kujenga vituo vya kupoza umeme kwenye Wilaya inayotekelezwa chini ya mradi wetu wa Gridi Imara. Mradi huo tayari umeshaanza na tunatarajia ndani ya miezi kama 12 kuanzia sasa mradi huo pia utakuwa umekamilika katika eneo la Uhuru ili kuhakikisha kwamba umeme unaotoka Tabora kwenda Uhuru kwenda Nguruka basi unawafikia wahitaji kwa wakati.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza napenda kuwapongeza viongozi wa TANESCO Mkoa wa Lindi na Kanda ya Kusini, kuna Mkurugenzi wa Kanda Eng. Makota, kuna Meneja wa Mkoa wa Lindi Eng. Kahinda na mameneja wa Wilaya zote Mkoa wa Lindi wamejitahidi sana kubadilisha hali ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Je, Serikali imejipangaje kuhakikisha Grid ya Taifa inapita katika Wilaya zote za Mkoa wa Lindi na Mtwara ili kuondoa adha hii ya umeme?

Swali la pili, gesi kwa asilimia kubwa inatoka Mkoa wa Lindi na Mtwara lakini wenyeji wa Mkoa wa Lindi na Mtwara mpaka sasa hivi wanatumia kuni na nishati ya mkaa kupikia. Je, Serikali haioni sasa ni wakati mwafaka wa kuwasaidia kuwapelekea umeme wananchi wale ili tuweze kulinda mazingira ya nchi yetu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwa niaba ya Wizara na Serikali kwa ujumla nipokee pongezi kwa ajili ya hawa watendaiji wa TANESCO ambao wanafanya kazi nzuri na wanajitahidi kuhakikisha kila eneo kwa kweli huduma ya umeme inakuwa ya kuimarika. Niwaahidi Waheshimiwa Wabunge kwamba sisi Serikalini na wizarani na wenzetu wa TANESCO tutaendelea kuhakikisha jambo hili tunalifanyia kazi kwa sababu ndio kazi yetu ambayo mmetuamini nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la pili kwa sababu Mkoa wa Lindi tayari unayo miundombinu ya umeme, tutakapokuwa tumefikisha Grid pale Masasi au Tunduru tayari Mikoa yote na Wilaya zote za Mkoa wa Lindi zitakuwa zimepata umeme wa Grid ya Taifa. Kitakachoendelea kufanyika ni kuendelea kusambaza umeme kwa kutumia miradi yetu ya REA kwenye vijiji na vitongoji ili kila mwananchi sasa aweze kupata umeme. Kwa hiyo, miradi hii mitatu mikubwa niliyoisema itakapokuwa imekamilika na Gridi itakuwa imeingia Mkoa wa Lindi na tayari kila wilaya itapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la pili kama tunavyofahamu sote Serikali imeanza sasa jitihada kubwa sana za kuhakikisha wananchi wote wanatumia nishati safi ya kupikia ambayo ni pamoja na gesi asilia, gesi za viwandani lakini pia na umeme, na katika maeneo yote ya Lindi na Mtwara tutaweka nguvu za ziada na jitihada kuhakikisha, zile nyumba chache ambazo tayari zimeunganishwa na gesi ya asili basi zinaongezeka kutoka kwenye idadi iliyopo kwa miradi ambayo tumeipanga kwenye bajeti inayokuja ili wananchi wengi zaidi waweze kutumia gesi asilia na hii mitungi mingine ya kawaida ya kuweza kupata nishati safi ya kupikia.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali na kwa hatua iliyofikiwa na hii itapelekea kukwamua hata makampuni makubwa na viwanda vikubwa ambavyo vilikwama kufunguliwa kutokana na kukosa umeme mkubwa. Pia kuna vijiji kadhaa na vitongoji kadhaa ambavyo vimekosa umeme kutokana na kuchelewa kwa mradi huu vikiwemo Vijiji vya Kata za Ulenje, Kinyara, Vijombe, Swaya, Igale, Iwindi na Bonde la Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; je, ni lini sasa Serikali itapeleka umeme kwenye Vijiji vya Ihango Kata ya Ulenje na Mina na Lusungo Kata ya Iwindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; je, Serikali ina mkakati gani wa kukwamua Mradi wa REA, awamu ya tatu, round ya pili, ambao umekwama kwenye Jimbo la Mbeya Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Oran Njeza kwa pamoja, kwa sababu yanahusu umeme vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Njeza pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote kwamba Mradi wetu wa Kupeleka Umeme Vijijini, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, utakamilika ifikapo Desemba. Vijiji aliyovitaja vilivyo katika kata hizo vyote vitakuwa vimepata umeme kufikia mwezi Desemba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mkandarasi anayepeleka umeme kwenye eneo la Mbeya Vijijini ni mkandarasi wetu ETDCO ambaye ni kampuni tanzu ya TANESCO na ameuliza ni jitihada gani zimefanyika kukwamua mradi kwenye eneo lake. Mkandarasi huyu sasa amewezeshwa zaidi na kampuni mama ya TANESCO, lakini na sisi kama Wizara tumeweka utaratibu mpya wa kusimamia miradi hii ikiwa ni pamoja na kuajiri vijana kwenye maeneo yetu ya majimbo, lakini kuajiri wakandarasi wahandisi wengi zaidi wa REA kwenye maeneo ya mikoa na kuweka ma - group ya kijamii ya WhatsApp, Waheshimiwa Wabunge wameyaona. Tunaamini kwa njia hizi na jitihada ikiwemo na kulipa pesa kwa wakati, miradi hii yote ya REA iliyokuwa inasuasua, itakamilika kwa wakati ikiwemo kwenye eneo la Mheshimiwa Njeza ambapo mradi utakamilika ifikapo Desemba kupitia makandarasi wetu wa ETDCO.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kunipa nafasi, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, lipo tatizo la umeme kukatika-katika hali inayosababisha vifaa vya umeme vinavyotumiwa na wananchi kuharibika.

Nini mkakati wa jumla wa Serikali kuhakikisha kwamba tatizo hili linaisha? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kuja Wilayani Kakonko kwa ajili ya kueleza mazuri sana haya ya Serikali ambayo Serikali inaendelea kuyafanya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru, naomba kujibu maswali mawili madogo ya nyongeza ya Mheshimiwa Aloyce Kamamba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli tunakiri kwamba bado kuna maeneo yanayo tatizo la kukatika umeme na maeneo mengine kukatika ni kwingi, maeneo mengine ni kudogo, maeneo mengine tumepunguza kwa sehemu kubwa. Eneo analolisema linayo line ya siku nyingi ya kilometa zaidi ya 280 inayohudumia maeneo ya Kakonko, Buhigwe, Kasulu na Kibondo ambayo sasa imeunganishwa na line ya Gridi ya Taifa inayotokea Nyakanazi kwenda mpaka maeneo hayo yenye kilometa takribani 25.

Mheshimiwa Spika, katika bajeti hii ambayo tunamaliza tumefunga kifaa kinachoitwa Auto Voltage Regulator ambacho kinaongeza nguvu ya umeme unaosafiri kwa muda mrefu ili angalau umeme uweze kufika mwingi kwa wadau mbalimbali. Katika bajeti inayokuja tumetenga pesa kwa ajili ya kwenda kuirekebisha na kuifanyia marekebisho makubwa hii line ikiwa ni pamoja na kubadilisha miti iliyochakaa, kubadilisha vikombe, lakini pia kubadilisha maeneo kidogo ya waya ambayo yamekuwa yakisababisha umeme kukatika kwenye maeneo haya.

Kwa hiyo, nimuahidi Mheshimiwa Mbunge kwamba katika kipindi kinachokuja cha mwaka wa fedha unaokuja katika kipindi kifupi ataona mabadiliko ya kurekebisha hii line ili iache kuwa inaathirika sana na matatizo ambayo yamekuwa yakitokea.

Mheshimiwa Spika, lakini katika eneo la pili, mimi niko tayari kwenda pamoja na yeye kuwaambia wananchi mipango mizuri kabisa ya Serikali, lakini pia na kusisistiza wao kushirikiana na Serikali katika kulinda miundombinu ambayo inapeleka umeme katika maeneo hayo, nakushukuru.
MHE. LUCY J. SABU: Mheshimiwa Spika, ahsante, Mkoa wa Simiyu una jumla ya vitongoji 2,649 lakini vitongoji 1,713 havijafikiwa na umeme; je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vitongoji hivyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, Serikali imekamilisha upembuzi yakinifu wa vitongoji vyote 36,101 vya Tanzania Bara ambavyo havina umeme, na tayari mradi umetengenezwa tunaouita kwa kifupi HEP – Hamlet Electrification Project na tunatarajia mwaka wa fedha wa 2024/2025 tutaanza kuutekeleza na utaigharimu Serikali jumla ya kama shilingi trilioni 6.7.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kuanzia katika mwaka wa fedha unaokuja Mkoa wa Simiyu, lakini kwenye majimbo yote mbalimbali yatapata vitongoji angalau 15 kwa kila jimbo. Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Lucy kwa kushirikiana na Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Bariadi anakotokea washirikiane ku-identify vile vitongoji 15 vya kuanzia ili kupunguza changamoto, lakini katika ule mwaka mwingine tutaanza sasa kupeleka umeme katika vitongoji vyote ambavyo vinahusika.
SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, hii bajeti tuliyopitisha ya juzi ni kama mlishauriwa kuangalia ukubwa wa majimbo, siyo? Maana jimbo lenye kata nne kwa mfano, linafanana na lenye kata 36, lenye kata 39, hapo itakuwaje hapo wote wanapewa 15 vijiji na mitaa ama? Maana mlituahidi, sasa hili ni jibu unatoa leo, mnaenda kuangalia na ukubwa wa majimbo au ukubwa wa majimbo utakuja 2024/2025?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa bajeti tuliyokuwanayo sasa na kwa uhalisia uliokuwepo tumeona kipindi hiki cha kuanzia iwe ni vitongoji 15 kwa kila jimbo kwa sababu ni mwaka wa fedha mmoja, lakini katika mwaka wa fedha 2024/2025 hivi vitongoji 36,101 vyote tunatarajia kuvipatia fedha. Kwa hiyo, kipindi hicho sasa tutaanza na wale wenye mahitaji makubwa zaidi tukielekea kwenye mahitaji madogo zaidi. (Makofi)

MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi, mimi leo nauliza je, ni lini sasa mtatupa jibu la uhakika la kutokukatika-katika umeme kwenye Jimbo letu la Temeke? Kwa sababu, mwaka 2021 hapa mlituambia mwezi wa Disemba umeme utakuwa sawasawa, mwaka 2022 mwezi Aprili utakuwa sawasawa, sasa ni mwaka 2023, je, ni lini? Tunaomba jibu la uhakika umeme kutokukatika-katika Temeke.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Kilave, Mbunge wa Temeke kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, sababu za kukatika umeme kwenye maeneo mbalimbali zinatofautiana. Wako ambao umeme unakatika kwa sababu miundombinu yao imepita kwenye maeneo ya mapori na inasongwa sana na miti. Wako wenye maeneo mengine umeme unakatika sana kwa sababu wako kwenye maeneo yenye radi na mvua kali kwa hiyo, zile radi zinaathiri vile vifaa.

Mheshimiwa Spika, yako maeneo mengine kama ya mjini ambako miundombinu imezidiwa na matumizi ya wananchi, lakini pia yako mambo mengine shughuli za kibinadamu za kugonga nguzo kwa magari na vitu kama hivyo vinavyosababisha matatizo hayo yatokee.

Nimuahidi Mheshimiwa Kilave kwamba kwenye mradi wetu wa Gridi Imara kwanza tunaongeza uwezo wa mitambo yetu wa kupeleka umeme kwenye maeneo mbalimbali, na yeye ni shahidi kwamba kwenye maeneo ya Temeke tumeanza kupitisha miundombinu chini kwa maana ya underground ili tupunguze zile habari za malori na magari mengine kugonga zile nguzo.

Mheshimiwa Spika, sasa mradi huu wa Gridi Imara pamoja na miradi mingine ambayo tunayo ambayo tayari umeshaona inatekelezwa tunatarajia itakapokamilika katika kipindi cha mwaka mmoja au miwili ijayo maeneo mengi sana matatizo ya kukatika kwa umeme yatakuwa yamekwisha, lakini yapo matatizo mengine madogo madogo ya transfoma imezidiwa kwa sababu wakazi wameongezeka kama maeneo ya Kariakoo na vitu kama hivyo, tunavifanyia kazi kwa kadri vinavyotokea. Tunaomba tuendelee kushirikiana kupeana taarifa pale changamoto zinapotokea ili tuweze kuzifanyia kazi.
MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi, Mkoa wa Katavi kwa ujumla una shida kubwa ya umeme kwa ujumla kwa sababu majenereta yaliyopo yameshindwa kuhimili idadi ya watu wanaotumia umeme. Serikali ina mpango gani wa dharura wa kupeleka jenereta litakaloenda ku-support umeme kwenye Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwanza Serikali katika mpango wa muda mrefu tunajenga sasa line ya kutoka Tabora – Ipole – Inyonga mpaka Mpanda Mjini kwa ajili ya kuhakikisha kwamba gridi imeufikia Mkoa wa Katavi, lakini katika njia za muda mfupi kama alivyouliza naomba baada ya hapa tutashauriana naye ili tuone tatizo ni kubwa kiasi gani na tuone ni wapi tunakoweza kupata mashine ya dharura ya kwenda kuongeza nguvu katika Mkoa wetu wa Katavi ili kipindi ambacho tunakamilisha upelekaji wa gridi basi wananchi waendelee kupata huduma ya umeme.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na niishukuru Serikali kwa majibu ya kutia moyo. Nina maswali mawili ya nyongeza: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye kaya nyingi kule Uchaggani na maeneo mengi ya Tanzania, kaya zote zina wanyama kama vile ng’ombe, mbuzi na kondoo: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwekeza kwenye gesi endelevu kwa mfano tupate nishati ya kupikia na kuwasha taa kutoka kwenye kinyesi cha wanyama ili kuzuia matumizi ya kuni?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; je, Serikali haioni umuhimu wa kuhamasisha wananchi watumie majiko bunifu na mikaa ya tofali inayotokana na pumba za mpunga na masalia mengine ya mimea ili kupunguza matumizi ya kukata miti na kuwapatia wananchi nishati?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Profesa Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru Mheshimiwa Prof. Ndakidemi, kwa ufuatiliaji wa eneo hili ambalo ni eneo jipya ambalo Serikali imetilia mkazo kuhakikisha kwamba tunatumia nishati safi, hasa ya kupikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijibu maswali yote mawili kwa pamoja kwa kutoa maelezo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tangu mwaka jana Mheshimiwa Rais alizindua mjadala wa Kitaifa wa nishati safi ya kupikia, na ni azma ya Serikali kupitia Wizara ya Nishati, mmeona tukijikimu kuelekea sasa kwenye nishati safi ya kupikia. Na katika eneo hili tunahamasisha utumiaji wa gesi ya mitungu, lakini gesi asilia, lakini pia maeneo mengine waliyoyasema ya kutumia biomass, kwa maana vinyesi vya wanyama, na mikaa hii ambayo ni ya kutengeneza ambayo haitoi moshi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Nishati kupitia REA inawezesha na ku-facilitate wale wagunduzi na watengenezaji wa majiko banifu na hii mikaa ya asili, kama mlivyotembelea mabanda yetu mliwakuta pale wabunifu wa namna hiyo. Kwenye Serikali itakuwa siyo rahisi sana kutumia nguvu ya Serikali kuzalisha umeme au gesi ya kupikia kwa pesa ya Serikali kutumia vinyesi vya wanyama na maeneo mengine. Kwa hiyo, Serikali inatoa pesa lakini pia tunapata mifuko mingine kama Green Fund ambayo ina-facilitate wananchi na wawekezaji binafsi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Prof. Ndakidemi kwamba tutaendelea kusimamia eneo hili kuhakikisha kwamba tunawawezesha wananchi na kuwapa fedha za mitaji ili waendelee kupata vitendea kazi vya maeneo hayo kuweza kuzalisha gesi asilia na kuweza kutumika katika kuwasha umeme, lakini pia katika nishati safi ya kupikia. (Makofi)
MHE. MARIAM N. KISANGI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa gesi asilia ina gharama ndogo sana kuliko ile gesi ya mitungi, na kwa kuwa Serikali imeshawekeza katika Mkoa wa Dar es Salaam, maeneo ya Mikocheni na Msasani: -

Je, Serikali ina mpango gani sasa kuhakikisha gesi hiyo asilia inapelekwa katika wilaya zote za Mkoa wa Dar es Salaam?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mariam Nassoro Kisangi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inayo azma ya dhati kabisa, na katika bajeti ya mwaka huu imetenga pesa kwa ajili ya kuendelea kupanua miundombinu ya upelekaji wa gesi asilia katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uunganishaji wa gesi asilia kwa mteja mmoja nyumbani kwake kwa miundombinu tuliyokuwa nayo sisi ina-range kutoka milioni mbili mpaka sita kwa mteja mmoja. Kwa hiyo, Serikali inaendelea kutafuta uwezeshaji wa kuweza kutambaza mabomba mengi zaidi katika maeneo yetu na kufikisha miundombinu hii ya gesi ili wananchi walio wengi zaidi waweze kupata nishati hii na kuitumia kwenye maeneo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili tumefungua milango kwa wawekezaji wengi zaidi ili waje washirikiane pamoja na Serikali kuweza kuendelea kusambaza gesi asilia katika Mkoa wa Dar es Salaam. Lakini tunao mpango wa kuleta mpaka Mkoa wa Dodoma na maeneo mengine ambayo wanaendelea kutumia na kuhitaji nishati ya gesi.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mikoa tisa iliyokabiliwa na ukame, Mkoa wa Simiyu ni mmoja wapo, je, Serikali ina mpango gani kupeleka gesi asilia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyojibu kwenye swali la msingi, gesi asilia inaweza kupelekwa kwa njia ya mabomba au kwa kugandamizwa na kuwekwa kwenye magari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa tuko katika Mikoa ya Dar es Salaam, Pwani, Mtwara na Lindi, lakini mipango iliyopo Serikalini ni kusogea sasa kuja katika Mikoa ya Bara kwa ndani zaidi kwa njia zote hizo, kwa maana ya kuwekeza katika kuleta kwa malori na treni au kuleta kwa bomba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Simiyu na maeneo ya Mkoa wa Mwanza ambapo kuna watumiaji wengi wanahitaji gesi kwenye viwanda, mipango ya Serikali ni kuendelea kupanua wigo wa upelekaji wa gesi katika maeneo hayo. Mkoa wa Simiyu nao pia utafikiwa pale ambapo uwezeshaji utakuwa umekamilika.
MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wengi wa vijijini wanatumia kuni na mkaa kwa sababu ndiyo nishati inayopatikana kwa wepesi kwenye maeneo yao: -

Serikali ina mkakati gani wa kupeleka nishati mbadala ambayo ni gesi asilia ili iendane na nguvu tunayotumia kupiga marufuku kutumia kuni na mkaa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Aida Joseph Khenani, Mbunge wa Nkasi Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kabisa kwamba watu wengi wa vijijini wanatumia mkaa na kuni katika hasa nishati ya kupikia. Tunalifahamu hilo na tumeliona na Serikali imeanza jitihada za kuanza kupunguza jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuanzia kwa namna ambayo imeonekana ni rahisi zaidi kuliko nishati ya gesi ya asili, ni kuwezesha wananchi kupata mitungi ya gesi ya viwandani kwa kuanza kupikia, na ninyi Waheshimiwa Wabunge ni mashahidi kwenye eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu wa fedha ilitengwa mitungu 70,000, tumetenga kwenye bajeti inayokuja mitungi takribani 200,000 ili angalau tutoe mtaji wa mwananchi kuweza kupata kianzio cha kupata gesi halafu baada ya hapo sasa ataanza kununua na kuelekea kwenye kutumia gesi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaboresha na kuona namna tunavyoweza kupunguza gharama za hii mitungi ya gesi ili wananchi walio wengi waweze kui-afford kwenye maeneo yao, Serikali inaweka ruzuku lakini tutaangalia namna nyingine ya kuweza kupunguza gharama hizi ili kila mwananchi aweze kutumia gesi safi ya kupikia.
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Kata za Eshkesh, Yaeda Chini na wakati unajibu swali mwaka jana ulisema mwezi wa saba ndiyo watapata umeme lakini sasa umepeleka mwezi wa 12. Je, huoni kwamba utakuwa unatucheleweshea kupata umeme katika Kata hizi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili Waziri ametupa vijiji kadhaa ambavyo vitapa umeme kama underline. Kwa sisi wa vijijini, vijiji vyetu lazima umeme upelekwe ndio uweze kupatikana umeme na kama utapeleka umeme katika maeneo ya underline peke yake ni kwamba sisi wa vijijini hatutapata umeme.

Je, Mheshimiwa Waziri uko tayari sasa kubadilisha kauli hii na mpango huu ili kuhakikisha sisi wa vijijini tupate umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulikuwa tunatarajia kumaliza mradi wa REA III Round II kwa awamu tofauti tofauti katika maeneo mbalimbali na sasa kwa walio wengi imekwenda mpaka Desemba mwaka huu na sababu kubwa ni mbili ambazo nyingine tulishazieleza huko nyuma za UVIKO na kuongezeka kwa bei za vifaa. Sababu nyingine iliongeza mwezi wa kumi wa mbili kuwa ndio deadline sasa ni kuongezeka kwa zile kilometa mbili ambapo Wakandarasi takribani wote 31 tayari wameshasaini ile mikataba ya kuongeza hilo loti kilometa mbili ili tuweze kuwa sasa kuwa na kilometa tatu za kupeleka umeme. Yote hiyo inatakiwa ikamilike kufikia mwezi Desemba.

Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Flatei pamoja na Waheshimiwa Wabunge wengine wote tusaidiane katika hili tumalize kazi hii ya upelekaji wa umeme katika vijiji vyote ifikapo Desemba mwaka huu ikiwa na extention ya hizo kilometa mbili.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili naamini alikuwa anazungumzia vitongozi japokuwa ametaja vijiji ambavyo viko underline, kwa sababu vijiji vyote vitakamilika Desenba mwaka huu. Tunafahamu kwamba tuna vitongoji 15 ambavyo tutapeleka kwa kila Jimbo. Kumekuwa kuna concern za Waheshimiwa Wabunge kwamba wapo ambao hawana vitongoji ambavyo viko chini ya line ambazo ni existing kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, Serikali sikivu ya Daktari Samia Suluhu Hassan tumerudi tena mezani kutizama namna ambavyo tunaweza tukapanua wigo wa mradi na tunatafuta aidha tupate pesa ya nyongeza au tubadilishe procurement process ili tuweze kupata vifaa na kuwapa Wakandarasi kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote.

Mheshimiwa Spika, hili tunalifanyia kazi na ninaamini litakuja na majibu mazuri katika muda mfupi ujao.
MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika Mji wa Kasulu lipo tatizo la umeme kukatikakatika wakati wa mchana na kurudishwa usiku. Je, ni lini tatizo hilo litakwisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, katika maeneo yote ambayo kuna tatizo la kukatikakatika kwa umeme tunafatilia sababu huenda ni kuongezeka kwa mzigo au ni kutotosha kwa umeme tutafuatilia na hapo ili tatizo hilo tulimalize lakini tunaamini tukifikisha gridi kubwa Mkoa wa Kigoma tatizo hilo litakwisha kwa upana wake.

MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Jimbo langu la Manyoni Magharibi vitongoji ambavyo viko underline havidi vitano.

Je, Serikali iko tayari sasa kutoa jibu la uhakika kwamba vitongoji katika Jimbo langu navyo vitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye swali la msingi tunatafuta mbinu mbadala ambayo itatuwezesha kupata mradi utakaofikia vitongoji 15 vilivyo underline na visivyo underline kwenye Majimbo yote.
MHE. VENANT D. PROTAS: Mheshimiwa Spika, ahsante katika vijiji vipya ambavyo mnapeleka umeme, kumekuwa na tatizo la Mkandarasi kufunga vifaa vilivyoko chini ya viwango na kusababisha umeme kukatikakatika na kukosa umeme zaidi ya siku 40.

Je, nini usimamizi wa Serikali kusababisha hili tatizo kutokuwepo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, vifaa ambavyo tunavifunga kule tunavihakiki kabla ya kuvilipa, inawezekana labda ni matumizi vimefika muda wake lakini nimwombe Mheshimiwa Mbunge tutashirikiana kuhakikisha kwamba tunahakiki tatizo hasa ni nini kama ni vifaa mbavyo havikidhi basi tuviondoe na mkandarasi arekebishe tatizo hilo.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi. Mkandarasi anayeitwa Giza anasuasua sana miradi yake katika Jimbo la Kiteto. Je, ni lini miradi ya umeme ya vijiji vya Kiteto itakamilika?

SPIKA: Ni Mkandarasi wa umeme halafu anaitwa Giza?

MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Spika, yes! Na miradi yake inasuasua.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mkandarasi Giza Cables ni mkandarasi anayetoka Misri na Misri kuna Mji ambao unaitwa Giza na ndio jina lake linapotokea na alikuwa anafanya kazi Manyara na Mara. Ameshakamilisha loti yake ya Manyara na kwa Manyara tunaendelea kumsimamia ili akamilishe kazi yake kabla ya Desemba atakuwa amekamilisha kazi hiyo.
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru ndani ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma Kata ya Chiwezi bado haijafikiwa na umeme. Serikali mna mkakati gani wa kuhakikisha wananchi wa Chiwezi wanapata huduma ya umeme? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, wananchi wa Chiwezi watapata umeme kabla ya mwezi Desemba mwaka 2023.

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, Serikali imefikia hatua gani kutafuta mkandarasi kwa ajili ya Visiwa vya Kilwa Kisiwani pamoja na Songo Mnara kupeleka umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, wenzetu wa REA wanakamilisha mradi wa kupeleka umeme katika visiwa ambao unajitegema tofauti na wa REA kwa sababu REA inaunganisha kwenye gridi, lakini maeneo ya visiwani bado hatujaweza kufikisha gridi lakini tunakamilisha kwenye visiwa takribani kama 358 vya kupelekea umeme. Mradi huo utakapokamilika Mheshimiwa Kassinge ataona tukiutekeleza.
MHE. TWAHA A. MPEMBENWE: Mheshimiwa Spika, nakushurukuru sana. Katikakatika ya umeme Jimbo la Kibiti, Rufiji, Mkuranga imekuwa ni donda sugu. Nini mkakati wa Serikali kukomesha tatizo hilo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Pwani ni Mkoa wenye viwanda vingi sana na unao-consume umeme mwingi zaidi, lakini tunahakikisha kwamba katika mradi wetu wa Gridi Imara tunautizama kwa karibu ili kuhakikisha wanapata umeme wa kutosha na wa uhakika na katika eneo lake la Kibiti tatizo hilo litakwisha.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na nimesikia majibu ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika vijiji ambavyo vimesalia nguzo zimepelekwa maeneo hayo na zimeachwa kwa muda mrefu na wananchi wamechukulia kwamba nguzo hizi zimetelekezwa; je, ni lini shughuli itaendelea kwa ukamilifu kuona nguzo zinasimikwa na vijiji hivi vinawashwa umeme?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, katika vijiji ambavyo vimepatiwa umeme, umeme umekuwa sio toshelevu hivyo wawekezaji kuvunjika moyo kushindwa kufanya shughuli zao zinazohitaji umeme mkubwa; je, ni lini Serikali itatuwekea capacitor au booster kwenye vijiji hivyo ikiwa ni sambamba na kujenga kituo cha umeme mkubwa kwenye Kata ya Nkangamo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Condester kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, kwenye hivi vijiji 20 ambavyo vimebaki kazi katika hatua mbalimbali zinaendelea. Mkandarasi anayefanya kazi katika Mkoa wa Songwe kwa ujumla anaitwa DEM, ni mkandarasi ambaye anaendelea kutekeleza kazi yake na katika mkoa yuko zaidi ya asilimia 80.

Mheshimiwa Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Condester kwamba kabla ya Disemba mwaka huu maeneo yote yatakuwa yamepatiwa umeme kwa sababu hatua ni moja moja kwenye maeneo tofauti tofauti, lakini nimhakikishe kwamba vifaa hivi ambavyo vimewekwa katika maeneo hayo ni vile ambavyo vitakuja kutumika katika maeneo hayo, havijatelekezwa na vitatumika kufanya kazi ambazo zinastahili kufanyika.

Mheshimiwa Spika, katika swali la pili, ni kweli kwamba kumekuwa kuna upungufu wa umeme katika maeneo mbalimbali na ni kwa sababu ya mahitaji kuwa makubwa na sisi kama Wizara ya Nishati tunaendelea kufanya assessment, na katika awamu hiiya kwanza ya Mradi wetu wa Gridi Imara tumetenga vituo vya kupoza umeme 15 katika maeneo mbalimbali kulingana na mahitaji makubwa yalivyo. Namhakikishia Mheshimiwa Condester pia kwamba nia ya Serikali ni kuhakikisha ifikapo angalau mwaka 2030 kila Wilaya iwe imepata kituo cha kupoza umeme kulingana na uwezekano wa upatikanaji wa fedha kutoka Serikalini, ili kuhakikisha kwamba tunafikisha umeme wa kutosheleza katika maeneo yote, lakini nimuombe baada ya hapa tutawasiliana ili tuone hilo eeo ambalo ni mahususi analolisema lina upungufu sana wa umeme saa hizi tulichukulie hatua mahususi na za haraka zaidi, ili kuwavutia wawekezaji zaidi.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Kijiji cha Mgwashi, Kata ya Lukozi wamekata tamaa kabisa na upatikanaji wa umeme baada ya kuwa wameahidiwa mara nyingi kwamba umeme unakwenda kuwashwa kwenye Kijiji chao. Naomba commitment ya Serikali, ni lini hasa Serikali itaenda kuwasha umeme katika Kijiji cha Mgwashi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema kwenye jibu la msingi nak ama ambavyo tumeeleza mara zote hapa, kabla ya Disemba mwaka 2023 vijiji vyote ambavyo havina umeme vitakuwa vimewashiwa umeme na Kijiji cha Mgwashi pia kitakuwa ni kimojawapo kitakachowashiwa umeme.

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Spika, Serikali iliahidi kwamba kufika tarehe 30 Juni, wananchi wa Ikomba watakuwa wamefikishiwa umeme wa REA, leo ninavyoongea hata nguzo zilizokuwepo kule wameziondoa; je, Serikali haioni kwamba haiwatendei haki wananchi wa Ikombe? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nimuahidi Mheshimiwa Jumbe kwamba, Mradi wa REA III, Round II unatakiwa kukamilika ifikapo Disemba, 2023. Yale maeneo ambayo bado hayajakamilika na nguzo pengine zimeenda zimepelekwa sehemu nyingine zitarudishwa zitapelekwa hapa, lakini nia ni kuhakikisha kwamba ifikapo mwezi Disemba, 2023 kila kijiji kimepata umeme na wananchi waweze kupata huduma hiyo, kwa hiyo, ahadi hiyo tutaitekeleza kwa kadri ilivyotolewa.

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, kwanza napenda nipate ufafanuzi zaidi kwenye jibu la msingi. Mkandarasi anayetekeleza mradi sasa hivi kule Rungwe ni ETDCO siyo State Grid Limited. Kwa hiyo, nilikuwa naomba nipate ufafanuzi zaidi kwamba, huyu State Grid Limited ameingiaje hapo? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Kwenye REA II kuna vijiji 25 viliachwa, vilitelekezwa, yaani kama viporo; napenda nijue kwamba ni lini huu Mradi wa REA II vijiji 25 utaanza kutekelezwa? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mkandarasi ETDCO ndio yuko site na Mkandarasi ETDCO anatekeleza Mradi wa REA III Round II. Ndiyo mradi unaoendelea ambao ni mkubwa ambao ETDCO anautekeleza na tunatarajia itakapofika Desemba atakuwa amemaliza kwa sababu, ni katika ile azma ya kuhakikisha vijiji vyote vinapata umeme ifikapo Desemba.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la pili sasa lililosema la vijiji 25 ambavyo vilikuwa vimeachwa na REA Awamu ya Pili tulikuwa tuna mabishano na mkandarasi kuhusu wigo wa utekelezaji na namna ya utekelezaji. Kuna maeneo alisimamisha nguzo, kuna maeneo aliweka waya halafu akaondoka, baada ya mvutano wa muda mrefu, ndiyo sasa tumemrudisha yeye mwenyewe, huyu huyu State Grid, ili aje kukamilisha vile vijiji vyake 25 ambavyo alikuwa ameviacha. Ndiyo maana tunasema ataanza Julai na atamaliza mwezi wa Kumi wakati ETDCO alianza tangu mwaka juzi, atamaliza Desemba mwaka huu.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye vijiji vya Kata ya Shizuvi ambavyo ni sehemu ya REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, vijiji vyote ambavyo viko kwenye Mradi wa REA Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, vitakamilika ifikapo Desemba mwaka huu wa 2023. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Oran Manase Njeza kwamba vijiji hivyo pia katika kata hizo vitakuwa vimefikiwa na umeme kabla ya Desemba mwaka huu 2023.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Katika vijiji 15 alivyovitaja vya vitongoji kumekuwa na changamoto kidogo kwa sababu, tulishapeleka vijiji 15 wakasema kwamba vijiji hivyo havitambuliki na TAMISEMI, lakini pia wakatoa condition nyingine kwamba vijiji hivyo lazima vipitiwe na mkondo mkuu wa waya.

Je, Serikali inatoa maelezo gani ya msingi kwa sababu inaonekana kule wale watendaji hawana uhakika wa kitu gani cha kutekeleza? (Makofi)

SPIKA: Nilikuwa najaribu kusikiliza kama swali lako linahusiana na swali la msingi au Hapana? Maana umetoa maelezo ya ziada hapo mwanzo yanayokuondoa kwenye swali la msingi. Swali lako ni nini? Uliza swali bila maelezo, itakusaidia kuwa kwenye swali la msingi

MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, vitongoji 15 alivyovitaja kwamba ndiyo vinatakiwa vipitiwe kwa ¬level hii ya umeme aliyoisema sasa hivi kunakuwa na mkanganyiko, wale watekelezaji hawajui kwamba watekeleze vipi? Kwa sababu, ukiwapelekea vitongoji wanasema ah, ah, vitongoji hivi havistahili kwa sababu, hakuna umeme. Sasa je, kuna condition ya vitongoji au hakuna condition kwamba, vitongoji vyovyote vinaweza kuwekewa au kuna condition fulani lazima ndiyo vipelekewe huo umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, katika vitongoji 15 ambavyo tumepata fedha ya kuvipelekea umeme katika mradi huu utakaotekelezwa mwaka 2023/2024 nieleze wazi kwamba ni vitongiji ambavyo tunaviita underline. Ni vitongoji ambavyo tayari miundombinu ya umeme mkubwa ilishapita katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, unakuta kwenye kijiji kimoja chenye vitongoji labda vitano, vitongoji viwili vimefikiwa na miundombinu kwa maana ya kuwashwa, kitongoji kimoja miundombinu imepita kwa juu haijashuka kwenye kile kitongoji na labda vitongoji vingine viwili havijafikiwa kabisa na umeme mkubwa na havijafikiwa na umeme mdogo.

Mheshimiwa Spika, fedha hii ndogo tuliyoipata Shilingi bilioni 379 inatosha kwa kupeleka miundombinu ya umeme mdogo tu katika yale maeneo ambayo tayari miundombinu ya umeme mkubwa ilishapita. Kwa hiyo, wale watendaji wenzetu kule chini wanayo maelekezo haya na wanajua namna ya kuwasilisha maelezo haya. Wataleta vile vitongoji ambavyo vilishapitiwa na line kubwa, sasa tunashusha umeme kwa ajili ya kujazia katika maeneo hayo. Pia mwaka 2024/2025 kwenye mradi wetu mkubwa wa HEP wa shilingi trilioni sita hapo tutakwenda kumaliza vitongoji vyote ambavyo vilishafikiwa na ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. Katika Kata ya Tarada, Kijiji cha Ngunga upo mradi wa nguvu za jua ambao ni wa gharama ya shilingi bilioni 275. Zoezi la kulipa fidia kwa waathirika bado limeanza kusuasua kutokana na changamoto ya migogoro ya maeneo.

Je, Waziri yuko tayari kufika katika eneo hilo ilimradi kutatua kwa haraka tatizo hilo na mradi huu uanze kutekelezwa kwa haraka? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ameuliza kama Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufika katika eneo hilo, ninayo hakika kwamba dhati ya moyo wake, lakini na sisi wasaidizi wake Wizarani tutafika na kuweza kuona tatizo ni nini kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Ardhi ili tuweze kulitatua. Kwa kuonesha nia ya dhati, tayari na mkataba wa utekelezaji wa mradi ule umeshasainiwa. Hivyo, hizi changamoto nyingine ambazo zitazuia utekelezaji hatuwezi kukubaliana nazo. Tutafika ili tutatue tatizo na mradi uanze mara moja.
MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa majibu ya Serikali na yanatia matumaini kwa wananchi, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza; mradi huu ulitegemewa kuwapatia umeme wa vijiji wanaopitiwa na mradi huu ikiwemo Vijiji vya Wambishe, Ihango katika Kata ya Ulenje na Vijiji vya Rusungomina katika Kata ya Iwindi na Bonde la Songwe ambako kuna viwanda vikubwa sana vinavyohitaji umeme mkubwa kwa ajili ya kuchakata madini. Sasa je, ni lini hawa wananchi watapatiwa umeme kwa mradi mbadala baada ya kuona huu mradi unasuasua?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, vilevile mradi wa REA III, awamu ya pili na mradi wa Densification umechelewa kwa kiasi kikubwa. Je, Serikali ina mkakati gani wa kunusuru hii miradi miwili ambayo ukiangalia mradi wa densification umepitwa na wakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze kwa kuendelea kufatilia mradi huu mkubwa tunaouita TAZA wa kupeleka umeme mkubwa katika maeneo hayo. Nimhakikishie tu kwa kauli ya Serikali kwamba mradi huu hausuisui, lakini ni taratibu za kimanunuzi zinazofanya mradi uonekane unachukua muda. Hata hivyo, kama tulivyosema kwenye jibu la msingi tayari taratibu za kufanya fidia zimekaribia kukamilika na kwenye mwaka wa fedha ujao tunatarajia kuanza kufanya fidia. Tayari wafadhili wameshapatikana na fedha ipo na ni taratibu za kukamilisha maandalizi ya utekelezaji wa mradi zinazoendelea na zitakapokamilika mradi utaanza mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongezee kwamba tayari vijiji hivyo alivyovitaja katika maeneo hayo viko katika program ya kupewa umeme na mradi huu. Tunayo program inayoitwa Land End Connection ambayo tunawaunganisha watu kwenye maeneo ya miradi mikubwa inapopita kama ambavyo wale wenzetu wanaopitiwa na mradi unaotoka Iringa kupita Dodoma, kupita Arusha kwenda Namanga walivyoona tukifanya kwenye maeneo hayo na huku pia tutafanya hivyo hivyo. Kwa hiyo niwaombe tu wananchi wa maeneo hayo wawe na matumaini na Serikali itawapelekea umeme katika maeneo yao baada ya kukamilisha taratibu za mradi ambao unatarajiwa kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, kuhusiana na REA ni kweli REA kama alivyosema siku chache zilizopita Mheshimiwa Waziri alipokuwa akijibu swali tulipata changamoto ya mabadiliko ya bei, lakini suala hilo tumelichukua kwa uzito wake kwa kukaa na wakandarasi na kukubaliana bei mpya zenye uhalisia kwa ajili ya kuendelea na utekelezaji wa mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, licha ya hayo, miradi hiyo katika maeneo mbalimbali inaendelea kwa hatua mbalimbali ya uthamini wa maeneo, ya kusimika nguzo, ya kuvuta nyaya kwa wale ambao walishapata vifaa hivyo kwa ajili ya utekelezaji. Kwa hiyo niwaonye, kuwaasa, kuwaomba, kuwashawishi na kuwashauri wakandarasi wote waendelee na utekeleaji wa miradi hii kwenye maeneo yao kwa sababu mikataba yetu ipo pale pale ili kuweza kufikisha azma yetu ya kukamilisha vijiji vyote vilivyobakia kwa wakati.
MHE. JESCA D. KISHOA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza kabisa kwa dhati ya moyo wangu napenda kuchukua fursa hii kuipongeza Serikali kwa nia yake ya kutaka kusitisha Mkataba huu mwaka 2024 ni jambo ambali nimelipigia kelele kwa muda mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya nyenzo muhimu sana na mahsusi kwa ajili ya kusaidia kutoingia mikataba ambayo haina tija katika Taifa ni pamoja na utekelezaji wa Sheria ya Tanzania ya Extractive Industry ya mwaka 2015 inayotaka mikataba yote ya sekta ya uzidiwaji kuwekwa wazi. Nataka kujua ni kwa nini kumekuwa kuna kusuasua kwa Sheria hii kutekelezeka?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili. Mkataba kati ya Serikali na Kampuni ya Songas ulioingiwa mwaka 2004 ni mkataba ambao unanyima fursa ya nchi ya Tanzania kunufaika na rasilimali kikamilifu. Nataka kujua Serikali imejipangaje mwaka 2024 kwenye mkataba mpya kuhakikisha kwamba hawafanyi makosa yaleyale kwenye eneo ya Investment cost, shareholding structure agreements na pamoja na eneo la capacity charges?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jesca Kishoa kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ninapokea pongezi alizozitoa kwa Serikali kwa jitihada ambazo zinafanyika pia ninamshukuru kwa kuuliza maswali ya msingi kabisa yenye ufuatiliaji na tija kwa watu wote wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na swali la pili kwamba Serikali imejipangaje. Kama nilivyosema kwenye jibu la msingi, tayari imeshaundwa timu ya kuanza kupitia mkataba uliopo sasa na kubaini ni wapi tuliteleza na kutibu hayo maeneo ambayo tuliteleza ili yasijitokeze tena.

Mheshimiwa Mwenyekiti, timu zipo nyingi, ipo timu iliyoundwa na TANESCO inaendelea na upitiaji, ipo timu iliyoundwa na Wizara inaendelea na upitiaji, ipo timu iliyoundwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali inaendelea na upitiaji. Kama tulivyosema kwenye swali la msingi mkataba unaisha Julai, 2024 na hii ni Mei, 2022, kwa hiyo tuna miaka miwili kufikia muda wenyewe wa kuisha kwa mkataba. Tunayo imani kwamba tutakuwa tumeshajipanga vizuri na kuona ni kitu gani tutakifanya kuhakikisha kwamba mikataba tutakayoingia itatupa tija sisi kama Taifa na kuhakikisha kwamba nia na azma ya kupeleka umeme kwa wananchi inafikiwa kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la kwanza la msingi la kwamba uwazi unakuwa guaranteed kiasi gani na Serikali. Niseme kama alivyosema kwenye Sheria ya Transparent Initiative ya Extractive Industry na umoja tuliokuwa taasisi tuliyokuwa nayo ya TEIT ambayo inasimamia uwazi na uwajibikaji katika mikataba hii, imekuwa ni shughuli inayoendelea nasi tunaji-subject kule kuweka mambo yetu wazi, kuonyesha wachimbaji au wadau katika eneo hilo wamekusanya pesa kiasi gani, wamepata faida kiasi gani, wamelipa kodi kiasi gani, tunaweka wazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupitia Bunge hili Kamati za Kudumu za Bunge zimekuwa zikiitisha mikataba hii, zimekuwa ziikitisha value for money areas, zimekuwa zikiitisha Wizara na maeneo mbalimbali kwenda kueleza kwao na kujua namna gani haya mambo yako wazi. Kupitia Bunge hili tunaamini wananchi wote sasa wanakuwa tayari kuona kwamba Serikali inafanya kitu gani kwa uwazi na uwajibikaji kupitia sisi Wabunge ambao tunakuwa kwenye Kamati mbalimbali. Kwa hiyo, niseme hata yeye Mheshimiwa Mbunge yuko na uhuru kupitia kwenye Kamati kuweza kupata taarifa mbalimbali zilizopo katika maeneo hayo. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nimemsikia Mheshimiwa Naibu Waziri anasema Serikali iko tayari kupitia mkataba tu ambao ameusema Mheshimiwa Jesca Kishoa. Lakini Wizara yenu ina changamoto nyingi tu ya mikataba mbalimbali ambayo inahusaina na umeme na inailetea hasara Taifa hili, ikiwepo ule wa Pangea na Mgodi wa Geita na maeneo mengine. Hamuoni kwamba kuna haja sasa kama Serikali kupitia mikataba yote ili kuona tumekosea wapi huko tunakoenda nchi yetu isipate hasara na iweze kurekebisha sasa hivi, ukiwepo na mkataba wa Bwawa la Mwalimu Nyerere? Ahsante.(Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mawazo na maoni yaliyotolewa kwa niaba ya Serikali niseme ninayachukua, tutaendelea kushirikiana Serikalini kwa ajili ya kushauriana namna bora ya kuweza kuwa tunafikia mikataba yenye tija kwa watu wote. Ile ambayo itakuwa imekwisha tutahakikisha tunafanya vizuri zaidi kwa nyakati zilizopo na ambayo inaendelea tutaona namna bora zaidi ya kuifanya iwe na tija kwa watu wote.
MHE. STELLA S. FIYAO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi pamoja na majibu ya Mheshimiwa Waziri, lakini naomba niwe na swali la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa Wizara imekuwa na utaratibu wa kufikisha huduma katika makao makuu ya vijiji na kusababisha watu wa vitongoji kukosa huduma.

Je, ni lini Wizara hii itaanza kufikisha huduma hii kwenye vitongoji ili wananchi wengi waweze kufikiwa na huduma hii ya Umeme? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba hatua ya kupeleka miundombinu ya umeme kwenye maeneo yote ya vijiji imekuwa ikienda awamu kwa awamu, ni kwamba tulianza na vijiji kidogo kulingana na uwezo wa Serikali uliokuwepo, lakini baadaye Serikali ikajihimu na kuhakikisha vijiji vyote vinafikishiwa miundombinu ya umeme angalau kwa kuanza na makao makuu ya vijiji. Lakini ipo mipango ya Serikali madhubuti kabisa ya kuhakikisha kwamba kila eneo linafikiwa na umeme na njia hizo ni kwa kuanza na miradi yetu ya ujazilizi inayoitwa densification ambapo tuna ya kwanza, ya pili na ya tatu zinaendelea, na zitaendelea kufanyika kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, lakini Serikali imeona ni vema kutafuta fedha nyingi kwa wakati mmoja na kumaliza vitongoji vyote ambavyo havijafikiwa na umeme na kama ambavyo tumeshasema mara kadhaa hapa Bungeni tumeona kwamba tunahitaji takribani shilingi trilioni sita na bilioni kama mita tano ili kumaliza maeneo yote ya vitongoji na Serikali ipo katika harakati za kuhakikisha kwamba inapata fedha hii kufikisha umeme katika maeneo hayo, lakini katika kipindi hiki cha kuanzia fedha inapopatikana Serikali inazidi kusogeza miundombinu ya umeme katika vitongoji kwenye maeneo yetu. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mbulu Vijijini kuna vitongoji 400 na vijiji 76; ulifika Mheshimiwa Waziri ukatoa ahadi vijiji vyote vitapata umeme.

Je, ni lini ahadi yako inatekelezwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei Massay kama nilivyojibu swali la msingi kwamba kadri Serikali inavyoendelea kupata fedha itajitahidi kuhakikisha kwamba vitongoji vyote vinapatiwa umeme katika muda mfupi ujao.
MHE. AGNES M. MARWA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana; Mkoa wa Mara ni kati ya Mikoa iliyokaa kimkakati ukizingatia ni Mkoa uliomtoa Muasisi Mwalimu Julias Kambarage Nyerere.

Je, ni lini Serikali itapeleka Umeme wa REA katika vijiji vyote vya Mkoa wa Mara ukizingatia wakati wakiomba kura Mama yetu Samia Suluhu Hassan na Hayati Magufuli waliahidi kwamba vijiji vyote vilivyobaki vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Agnes Marwa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hivi tunavyozungumza mradi kabambe wa kupeleka umeme kwenye vijiji unaoitwa REA III Round Two unaendelea katika vijiji vyote nchini, na Mkoa wa Mara ni mmojawapo kati ya maeneo hayo. Na ninakumbuka mkandarasi anayepeleka umeme katika maeneo haya anaitwa Giza Cables, anapeleka umeme katika Mikoa ya Manyara na Mara, na tunatarajia kufikia Desemba mwaka huu vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme vitakuwa vimefikiwa na umeme kwa mkataba tuliokuwa nao na tunasimamia kwa karibu kabisa kwa sababu pesa tunayo na kazi inaendelea.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, katika vijiji ambavyo vilipatwa na changamoto ya umeme kutokukamilika ni vijiji takribani vyote vya kata kama tatu hivi katika Jimbo la Lulindi; Kata ya Mchauru kulikuwa na hiyo; Kata ya Sindano, Kata ya Luatala.

Je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha vijiji hivi vilivyokosa umeme mpaka sasa hivi katika kata hizo na maeneo mengine ya Lulindi vinapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mchungahela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nikwamba ifikapo Desemba, 2022 Serikali imeji-commit kuhakikisha inafikisha miundombinu ya umeme katika vijiji vyote Tanzania Bara ambavyo havijafikiwa na umeme na kazi zinaendelea katika maeneo mbalimbali, wakandarasi wako site wanaendelea.
MHE. JAPHET N. HASUNGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa kuwa katika Jimbo la Vwawa kuna vijiji 31 ambavyo bado havina umeme, na kwa kuwa mkandarasi sasa hivi karibu mwaka mmoja umekatika hakuna kijiji hata kimoja ambacho kimepata umeme.

Je, Serikali inatuhakikishiaje kwamba kufikia Desemba vijiji vyote hivyo vitakuwa vimewashwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Japhet Hasunga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, taratibu za kupeleka umeme wa REA na miradi mingine mikubwa uko katika awamu tofauti tofauti na kwa harakaharaka tunayo awamu ya kumpata mkandarasi na tukishasaini mkataba anakwenda site kufanya physical verification, anakwenda kukagua maeneo na kuona uhalisia wake, lakini tunarudi mezani yeye pamoja na TANESCO na REA kuangalia na kukubaliana scope ya kazi yenyewe ambayo inatakiwa ifanyike halafu anakwenda kwenye hatua ya tatu ya kuagiza vifaa na hatua ya nne ni ya kwenda site na kuanza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, ninaamini kabisa kwa Mheshimiwa Japhet Hasunga mojawapo au mbili au tatu ya hatua hizo zinaendelea, na tunatarajia ifikapo Desemba muda wa kufanya kazi kwa miezi hii sita, saba iliyobakia tutakabana na wakandarasi kuhakikisha kwamba tunafikisha huduma hii ya umeme kwenye maeneo yote kwa sababu tayari vifaa vimeshanunuliwa na surveys zilishafanyika na sasa wako site wanaendelea kufanya kazi, kwa hiyo kazi zitakamilika. (Makofi)
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kule kwenye Jimbo la Tarime Vijijini eneo la Nyamungo na Nyamwaga wananchi wangu wamekwenda kulipia nguzo za umeme wa REA badala ya kulipia shilingi 27,000 wamedaiwa shilingi 515,000 kwa nguzo moja.

Naomba nipate kauli ya Serikali kwamba bei imebaki shilingi 27,000 ile ambayo tulikubaliana kwa wananchi wetu au kuna mabadiliko mengine sasa ya gharama ya umeme wa REA? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwita Waitara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bei za umeme za maeneo ya vijijini ni shilingi 27,000 bila kujali habari ya nguzo au transfoma au nini; kwa vijijini ni shilingi 27,000. Maeneo ya mijini ndiyo yamerudia kwenye zile bei ambazo tayari Serikali inaweka ruzuku ili ziweze kuwa za chini kidogo ili wananchi waweze kuzikimu, lakini kwa vijijini ni shilingi 27,000.

MHE. MOHAMED L. MONNI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Spika, Kituo cha Afya cha Bakorongo kilikamilika na kufunguliwa na Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete, mwaka 2007, tangu hapo maelekezo yamekuwa yakitolewa kiwekewe umeme na hakijawekewa.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua nini kauli ya Serikali kuhusu kuweka umeme katika kituo hicho cha afya? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tunayo maeneo mengi ya taasisi za umma ambayo hayajafikiwa na umeme, kwenye vituo vya afya, vyanzo vya maji, shule na taasisi za dini. Baada ya kuona mahitaji makubwa wenzetu wa REA wamekuja na mkakati na mradi maalum ambao tutapeleka umeme katika vyanzo vya maji, vituo vya afya na migodi ili kuharakisha na kurahisisha ufikaji wa miundombinu ya umeme katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, naomba baada ya kutoka hapa basi nizungumze na Mheshimiwa Mbunge ili tuone kama liko captured kwenye huo mradi wetu ambao tunatarajia unaweza ukaanza mwishoni mwa mwaka huu. (Makofi)
MHE. MIRAJI J. MTATURU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi nami niulize swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Tarafa nzima ya Mungaa katika Jimbo la Singida Mashariki nilishasema hapa haina umeme hata kijiji kimoja. Lakini juhudi zilifanyika, kata nne zimeshawekewa nguzo leo ni mwezi wa nne unakwenda wa tano.

Ni lini sasa mkandarasi atarudi kuja kuweka nyaya na transfoma ili wananchi wale waanze kupata umeme wakati wengine wanasubiria kumalizia nguzo zilizobaki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mtaturu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kulitokea changamoto ya ongezeko la bei, hasa kwenye bidhaa za vyuma, copper na aluminium ambazo zinatumika kutengeneza transfoma, nyaya na accessories nyingine katika uunganishaji wa umeme.

Katika kujadili tatizo hili na kulitatua imetuchukua kidogo muda, lakini tunakaribia kumaliza jambo hili na tunaamini mwishoni mwa mwezi huu basi habari ya kuvuta waya, kufunga transfoma na mengine yataendelea kwenye maeneo ambayo tayari nguzo zilishasimamishwa. Na ninaelekeza kwa wakandarasi yale maeneo ambayo bado nguzo hazijasimama basi kazi zisizohusika na ongezeko la bei ziendelee kufanyika wakati mambo mengine haya yakiendelea kukamilika, kuhakikisha kwamba umeme unafika kwa wakati.
MHE. CONSTANTINE J. KANYASU: Mheshimiwa Spika, Jimbo la Geita Mjini kata nane hazijafikiwa na umeme mpaka leo. Serikali iliahidi kwamba kutakuwa na mradi wa peri urban ambao ungeanza mwezi Aprili, lakini leo ni mwezi Mei mradi huo haujaanza. Ni lini mradi huo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Constantine Kanyasu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kuna maeneo ambayo yako mijini lakini yana muonekano wa kuwa vijijini, ukiachana na kwake Geita, hata Jimbo ninalotoka mimi la Bukoba Mjini lina hali hiyo hiyo; na ni kweli Serikali iko katika harakati za mwisho za kukamilisha Mradi wa peri urban ambao tunatarajia utaanza kufikia mwezi Julai ili kupeleka umeme katika maeneo ya mijini, lakini yenye muonekano wa vijiji.

Nimuombe Mheshimiwa Mbunge awaambie wananchi wavumilie kidogo, Serikali ya Awamu ya Sita itatimiza ahadi yake na mimi nimo humohumo.
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniona.

Mheshimiwa Spika, kata tatu za Kilolo yaani Ukwega, Nyanzwa na Udekwa, hazina umeme, na mkandarasi alikuja akachomeka nguzo, sasa ni miezi sita haonekani.

Je, Serikali iko tayari kumuita na kumtafuta huko aliko ili aende akamalizie ile kazi kule? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nyamoga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli eneo moja na eneo lingine hatua za utekelezaji zinatofautiana kulingana na mkandarasi alianza lini na amepata vifaa wapi na mambo kama hayo na kama nilivyoelekeza wakandarasi wote waendelee na kazi zisizohusiana na mazungumzo tunayoyafanya kuhusiana na bei.

Mheshimiwa Spika, naomba nikitoka hapa niwasiliane na Mheshimiwa Nyamoga ili nione hasa kwake kuna changamoto gani mahususi ili kama ni kuitatua mara moja tuitatue, kama ni ile ambayo inaendelea kwenye taratibu nyingine basi namhakikishia kwamba kazi itaendelea na itakamilika kwa wakati.
MHE. FURAHA N. MATONDO: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilitangaza mabadiliko ya bei za umeme kwa wananchi wanaoishi mjini. Wananchi wanaoishi pembezoni mwa mji mfano Kishiri, Sangabuye, Buhongwa na Kayenze na tayari walishalipia umeme wa shilingi 27,000.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwawekea umeme? Walishalipa kabla ya tangazo la Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kutoa majibu kwenye swali la nyongeza la Mheshimiwa Furaha kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, naomba kusema maneno machache yenye uhalisia na ukweli; wale wote waliokuwa wamelipa shilingi 27,000 kabla ya mabadiliko ya bei wataunganishiwa umeme kwa gharama ya shilingi 27,000. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, agizo hili liko kwa Mameneja wote wa Mikoa na wa Wilaya na wanajua, na tulikubaliana kuwa wale wenzetu waliokuwa wametangulia kulipa wapewe kipaumbele kwa kufanya first in first out. Kwa hiyo wale ambao bado hawajaunganishiwa na walishalipa shilingi 27,000 wasiwe na wasiwasi gharama italipwa na wale ambao wanaona wamechukua muda mrefu naomba tuwasiliane ili tuweze kuona tatizo na changamoto iko wapi ili tuweze kuondokana na tatizo hili.
MHE. GEORGE N. MALIMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru, nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza, pamoja na ujenzi wa njia mpya ya kusambaza umeme bado upatikanaji wa umeme katika Wilaya ya Mpwapwa na hasa maeneo ya vijijini siyo ya kuridhisha. Ni nini tamko la Serikali juu ya kuondoa tatizo hili kabisa? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; ni lini Serikali itaanza zoezi la kubadilisha nguzo za miti ambazo zimekaa kwa miaka mingi na nyingi zimechakaa na kuanza kuweka nguzo za zege? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa George kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nianze na la pili kama nilivyosema kwenye jibu la msingi kuanzia mwaka wa fedha ujao, fedha imeshatengwa, itatengwa na kwa ajili ya kuweza kubadilisha nguzo zilizochakaa kuweka za zege, waya na vikombe na maeneo kama hayo.

Mheshimiwa Spika, kwenye swali la kwanza; kwanza nipende kuwaambia Waheshimiwa Wabunge kwamba tarehe moja na tarehe mbili tutaleta habari njema ya faraja kwa Watanzania kutoka kwa Mheshimiwa Rais kupitia bajeti ambayo tutakuja kuisoma hapa ikiwa imetengwa takribani shilingi bilioni 500 kwa ajili ya kuboresha Gridi ya Taifa na maeneo yanayohusika na Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye eneo hili, eneo la Mpwapwa litapata maendeleo ya ziada kwa sababu imetengwa pesa kwa ajili ya kujenga kitu kinaitwa switch station pale Mbande ambacho sasa kitapunguza urefu wa njia ya kutoa umeme Zuzu kwenda mpaka pale na tukishakijenga station pale Mbande itatoka na njia nne mojawapo itakuwa ikienda Mpwapwa. Kwa hiyo, itafikisha umeme kwa urahisi na utakuwa ni umeme mkubwa.
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nina maswali mawili ya nyongeza. Lakini Shirika letu la Umeme TANESCO Ta rime linafanya kazi nzuri ya kusambaza umeme ingawa wanafanya kwa mazingira magumu hawana gari. Ningeomba Serikali wawapatie gari ili warahisishe usambazaji wa umeme katika Mji wetu wa Tarime.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kumekuwepo na utamaduni wa kurundika nguzo katika mitaa na nguzo hizo zinakaa muda mrefu kwa mfano katika Mtaa wa Ugete kuna nguzo zimekaa pale miaka miwili sasa na mpaka sasa hazijasambazwa. Je, ni lini nguzo hizi zitasambazwa ili wananchi waweze kupata umeme? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, kumekuwepo na utamaduni wa kupeleka umeme katika kaya moja katika mtaa. Kwa hivyo kaya nyingi katika mitaa hiyo inayofata haina umeme. Ni lini Serikali itasambaza umeme katika kaya hizi ambazo hazijapata umeme katika mitaa hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Michael Kembaki Mbunge wa Tarime Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikubali kwamba, miundombinu na vitendea kazi tulivyokuwa navyo havitoshi lakini Serikali inaendelea kujihimu na katika bajeti inayokuja tunataraji kupata magari na vitendea kazi vingine na kuvisambaza katika maeneo yenye uhitaji kwa ajili ya kuweza kuwezesha utendaji wa kazi nzuri. Naamini na Tarime Mjini pia itanufaika na matengenezo na mafanikio hayo ambayo tutakuwa tumeyapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye maswali mawili ya nyongeza nimwakikishie Mheshimiwa Kembaki kwamba katika bajeti inayokuja tumetengewa fedha za kutosha na Mheshimiwa Rais ametuhakikishia kuzipata kwa ajili ya kukamilisha hiyo miradi ambayo imekuwa ni viporo kama inaonekana nguzo zimelala miradi haijakamilika lakini na kuongeza wigo wa kupeleka umeme katika maeneo yetu kuanzia kwenye maeneo ya vijiji pia kwenye maeneo ya mitaa. Kwa hiyo, tutakuwa na nafasi nzuri ya kupanua wigo wa kupeleka umeme kwenye maeneo mbalimbali kuanzia mwaka ujao wa fedha kwa sababu tunatarajia kupata fedha nyingi zaidi.
MHE. ESTHER L. MIDIMU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Ni lini Serikali itasambaza umeme katika vijiji 202 vya Mkoa wa Simiyu vilivyobaki ili viweze kupatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Midimu Mbunge wa Mkoa wa Simiyu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba tayari REA III Round II inaendelea katika maeneo yote ya Tanzania katika maeneo ya vijiji ambavyo havikuwa na umeme na tunaamini kufikia Desemba tutakuwa tumekamilisha kwenye baadhi ya maeneo na wengine wataendelea kukamilisha kwa mujibu wa ratiba walizokuwanazo. Kwa hiyo, umeme katika eneo lake utaendelea kupelekwa na kuwafikia wananchi.
MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, tatizo lililoko Tarime Mjini ni sawasawa na tatizo lililoko kwenye Halmashauri ya Msalala. Kwa kuwa Serikali imekuwa ikitumia fedha nyingi kupeleka umeme kwenye makao makuu ya vijiji na hivyo kupelekea baadhi ya mitaa kukosa huduma ya umeme. Ni lini Serikali itaanza umeme kwenye mitaa ya Kata ya Bulyamuru, Segese, Isaka na Burige?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tulivyosema kwenye jibu la msingi mitaa yote ambayo haijafikiwa na umeme katika mwaka wa fedha unaokuja, tunayo program yetu ya Densification 2B na 2C itahakikisha inafikisha umeme katika maeneo hayo kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.
MHE. NICODEMAS H. MAGANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, naomba kuuliza Mkandarasi wa Mbogwe aliripoti toka mwaka jana lakini mpaka sasa hivi hakuna kazi inayofanyika, vijiji 34 havijapatiwa umeme. Ni nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maganga Mbunge wa Mbogwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi ya REA III Round II inaendelea katika hatua mbalimbali katika maeneo yetu, kama ambavyo tumewahi kueleza hapa Bungeni kwamba miradi ya REA III round II inazo hatua kadhaa za kufikia ili kuweza mradi kukamilika katika utekelezaji wake. Kwa hiyo, nimwakikishie Mheshimiwa Maganga kwamba naamini katika eneo lake hatua mojawapo katika mradi huo itakuwa inaendelea. Lakini nimwombe kwa sababu lipo banda letu hap ana mkandarasi anayetengeneza mradi huo yuko hapa, Meneja wa Wilaya yuko hapa, Meneja wa Mkoa yuko hapa basi tutembelee pale na tuweze kujua tatizo na kero ambazo zipo.
MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Mheshimiwa Waziri Kata ya Lahoda, Sanzawa- Mpendo na Kinyamshindo zilikuwa zipate umeme REA phase II lakini hazikufanyiwa hivyo. Na sasa tuko kipindi cha REA phase III. Nini mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kata hizi na vijiji vyake vinapata umeme katika Mradi huu wa REA phase III? ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Majala kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya REA III round II kuisha ninatoa maelezo ya Serikali hakuna Kijiji kitakuwa hakijafikiwa na Nishati ya Umeme. Commitment ya Serikali ni kuhakikisha kwamba katika awamu hii ya tatu mzunguko wa pili vijiji vyote Tanzania Bara vinapata umeme. Kwa hiyo, nimwakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo hilo pia litapata umeme.

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, kwanza niseme tu kwamba sijaridhika na majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri kwa sababu hata maeneo ambayo ameyataja hapa kwamba yamejengewa ofisi kwa mfano mimi kwenye Jimbo langu hakuna kata inayoitwa Bulungwa wala Chambo.

Sasa Mheshimiwa Waziri niseme kwamba ni lini sasa mtaanzisha ofisi hizo ambazo wewe umezitaja hapa ikiwemo Kata ya Isaka, Kata ya Segese, Kata ya Bulige na Kata ya Jana? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili la nyongeza wakati mnaendelea kufanya upembuzi yakinifu au tathmini, Mheshimiwa Waziri alifanya ziara kwenye Halmashauri ya Msalala na tukampatia kiwanja na tofali 1000 na akaahidi kujenga ofisi kwenye Halmashauri ya Msalala.

Sasa ni lini Serikali mtaanza ujenzi wa ofisi ya Wilaya kwenye Halmashauri ya Msalala? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nikianza na swali la pili la ni lini Serikali itaanza kujenga ofisi; kama tulivyoeleza kwenye jibu la msingi TANESCO inaendelea na tathmini mahitaji ya vigezo kwa ajili ya kufungua ofisi hiyo, kwa hiyo tathmini itakapokamilika mara moja mahitaji yakabainika ni kwa kiasi gani basi itaamuliwa ijengwe hiyo ofisi kwa mazingira yatakayo kuwepo.

Mheshimiwa Spika, lakini kweli swali la kwanza kwamba ofisi hazijafunguliwa; kwa sababu ya uhaba wa watumishi tuliokuwa nao na kwa sababu ya ufinyu wa bajeti ya kujenga majengo yetu katika maeneo yote wenzetu wa TANESCO walianzisha utaratibu wa kufanya visiting offices ambazo ni katika haya maeneo ya hizo ofisi ndogo tukiazima maeneo ya ofisi za kata. Kwa hiyo, maeneo haya hautaenda na kukuta jengo limejengwa lakini tunapata vyumba kwenye ofisi za watendaji wa Kata na tunaanza kuhudumia watu kutokea kwenye maeneo hayo, wakati Serikali ikiwa inajihimu kuongeza bajeti kwa ajili ya kuweza kujenga majengo hayo kwenye maeneo yote yanayohitajika. (Makofi)
MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Moja ya sababu za kujenga ofisi na kupeleka vifaa ni pamoja na kuhakikisha huduma ya TANESCO inakuwepo kwa wananchi; sasa pale Halmashauri ya mji wa Bunda tuna ofisi lakini bado hamjaweza kutoa huduma stahiki ya umeme, watu wameomba maombi ya umeme, wana control number, lakini mpaka leo hawajaunganishiwa umeme.

Ni lini mtahakikisha huduma bora inaenda kwa wananchi na sio tu ofisi peke yake?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ester Bulaya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika bajeti tutakayoisoma hapa siku chache zijazo itaoneshwa ni kwa kiasi gani Serikali ya Awamu Sita imejipanga kuwahudumia wananchi kwa kuongeza fedha kiasi zaidi ya bilioni 500 kwa ajili ya kupeleka huduma kwa wananchi. Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya siku mbili ataona neema iliyoshushwa na Mheshimiwa Rais kupitia Wizara ya Nishati. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kazi ya usambazaji umeme kwenye vijiji ambavyo Mheshimiwa Naibu Waziri amevitaja unaendelea, lakini hata hivyo kazi hii bado inafanyika kizamani, kwa maana ya kwamba inafanyika tu sehemu kubwa ya makao makuu ya kata. Lakini inasababisha sasa kwa mfano Kijiji cha Mumburu A na B kwenye vitongoji vya Chalinze na Mtakuja. Lakini pia Chipite, Mkang’u, Mwongozo na Nganga A Shule ya Msingi, Mbemba pamoja na Namali kazi ya kuweka umeme inafanyika kwenye maeneo madogo sana, kwa maana ya scope.

Mheshimiwa Naibu Spika, je, Wizara haioni kuna haja maeneo mapya wanapoweka umeme wakafanya kazi kubwa tofauti na ilivyokuwa zamani wanapeleka nguzo 20 tu?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwenye Wilaya yetu ya Masasi kumekuwa na tatizo kubwa sana la kukatika katika kwa umeme na Serikali hii ilituahidi kwamba itatengeneza line ya pekee kutoka Maumbika mpaka Masasi kwa bajeti ya shilingi bilioni 10. Nataka nifahamu kutoka kwa Mheshimiwa Naibu Waziri, kazi hiyo inakusudiwa kuanza lini? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Cecil David Mwambe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kwenye swali la kuongeza wigo wa upelekaji wa umeme kwenye vitongoji, nikiri kwamba kweli bado tunavyo vitongoji vingi ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme, lakini Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan imejitahidi kwa kuanzia na mradi wa REA III round two kwa kupeleka umeme kwenye vitongoji vya kuanzia katika vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo tumeshasema hapa mara kadhaa, Serikali inatafuta pesa ya kutosha kabisa kuweza kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote nchini vilivyobakia takribani trilioni sita zinahitajika kwa ajili ya kukamilisha kazi hii na hatua za kuendelea kutafuta pesa hiyo zinaendelea na tunaamini chini ya uongozi wa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan tutafanikiwa kwa jambo hilo katika muda mfupi unaokuja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye swali la pili, ni kweli Serikali iliahidi kujenga njia ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Maumbika kuja mpaka Masasi na tayari upembuzi umeshafanyika na pesa imeshapatikana na katika bajeti ambayo tunaisoma hapa kesho kipande hicho ni kimoja wapo katika ambavyo tunaviahidi kuvitekeleza katika mwaka wa fedha unaofuata. Nashukuru.
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru; ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji vya Jimbo la Singida Magharibi ikiwemo Kintataa, Irisia na Mwasutianga? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kuna baadhi ya vijiji ambavyo havikuwa vimefikiwa na miundombinu ya umeme lakini Mradi Kabambe wa Upelekaji wa Umeme Vijijini, Mzunguko wa Tatu, Awamu ya Pili, utakamilisha vijiji vyote kufikia Desemba mwaka huu kwa mikataba tuliyokuwa nayo. Kwa hiyo na vijiji alivyovitaja Mheshimiwa vimo katika mpango huo na vitapelekewa umeme.
MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; nina vijiji 27, vitongoji zaidi ya 300 katika Jimbo la Tarime Vijijini vikiwepo Magoma, Kitenga, Masurura, Gibaso, Nyabitocho, Kebweye, Korotambe, Kegonga, Mosege, Kihongera na Soroneta. Wananchi hawa waliahidiwa kwamba mwaka jana mwezi Desemba umeme ungeweza kuwaka mpaka sasa haujawaka. Mheshimiwa Naibu Waziri ana kauli gani katika maeneo haya ya kupata umeme? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Waitara kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi yetu ya kupeleka umeme vijijini Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili inaendelea katika vijiji vyote nchini ambavyo havikuwa vimefikiwa na miundombinu ya umeme na tunatarajia kuanza Desemba tutaanza kukamilisha miradi hii, na upelekaji wa umeme katika vijiji na vitongoji upo katika hatua mbalimbali.

Kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Waitara kwamba vijiji hivyo viko katika taratibu za kupelekewa umeme na kufikia Desemba tunaamini tutakuwa tumekamilisha mradi wa kupeleka umeme kwenye vijiji hivi.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi; je, ni lini Serikali itaunganisha Mkoa wa Kigoma na Gridi ya Taifa?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Dkt. Florence Samizi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kigoma ni mmoja wapo kati ya mikoa michache iliyokuwa imebakia bila kuunganishwa na Gridi ya Taifa, na nimpe taarifa na habari njema ya Serikali ya Awamu ya Sita kwamba kabla ya mwezi Oktoba mwaka huu Gridi ya Taifa itakuwa imeanza kufika Kigoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, na tutapeleka Gridi ya Taifa Mkoa wa Kigoma kwa njia nyingi, naomba uniruhusu nizitaje kwa haraka haraka; tunaanza na njia ya msongo wa Kv33 kutoka katika Kituo cha Kupoza Umeme cha Nyakanazi kwenda Kakonko – Kibondo – Kasulu mpaka Kigoma Mjini, na hiyo itakamilika mwezi Agosti. Kuna njia ya msongo wa Kv 400 ambayo inajengwa kutoka Nyakanazi kwenda mpaka Kigoma, mkandarasi wa TATA yuko site; lakini kuna njia ya msongo wa kv 400 inayotoka Sumbawanga kuja kuingia mpaka Kigoma, na yenyewe itapeleka pia umeme wa Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, habari njema zaidi ni kwamba tunajenga mradi wa kuzalisha umeme katika Mto Malagarasi (megawati 49.5), kufikia mwaka 2025 utakuwa na wenyewe umefikisha umeme.

Mheshimiwa Naibu Sapika, nashukuru.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na matatizo ya kukatikakatika kwa umeme mara kwa mara katika Jimbo la Kinondoni na mara nyingi sana bila hata taarifa kutoka TANESCO.

Ni nini kauli ya Serikali katika kuondoa tatizo hili ili wananchi wa Kinondoni waweze kuishi kwa amani na kupata huduma hii?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Tarimba, Mbunge wa Kinondoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli kabisa jitihada kubwa zimefanyika katika siku chache zilizopita na imepunguza sana kukatikakatika kwa umeme katika maeneo mengi sana nchi. Lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti inayokuja, Serikali imetenga pesa ya kutosha kwa ajili ya kurekebisha vituo vya kupoza umeme, kuongeza ukubwa wa transfoma tulizonazo, kurekebisha miundombinu ya umeme kama nyaya na nguzo na hivyo tuna uhakika kwamba kufikia mwishoni mwa mwaka wa fedha ujao matatizo ya kukatika kwa umeme yatakuwa kama siyo kuisha, yamepungua kwa asilimia kubwa kabisa.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale Musoma Mjini, Mitaa kama Bukoba, Songambele, Zanzibar na kule Bukanga mwaka mmoja nyuma ilikuwa inapata umeme wa shilingi 27,000 kwa sababu ni mitaa ya pembezoni. Lakini kwa sasa hivi tayari mambo yamegeuka, wanalipa zaidi ya shilingi 300,000 ambapo wananchi wengi hawana uwezo.

Je, nini kauli ya Serikali kuhusu kuendelea kuwaruhusu waendelee kulipia umeme kwa bei ya shilingi 27,000 kama ilivyokuwa awali?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mathayo Manyinyi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na changamoto ya tafsiri na utekelezaji wa gharama za kuunganisha umeme kwa wananchi, na kwa haraka haraka kuna watu wako maeneo ya mijini na wanaonekana wako mijini lakini hali zao za kiuchumi haziwezi kukidhi malipo ya gharama kubwa ya kuunganisha umeme. Lakini vilevile kuna watu wanaonekana wako maeneo ya vijijini, lakini hali zao za kiuchumi ni kubwa na wanaweza wakalipa zile gharama kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuonekana kuna changamoto hiyo tumepata maelekezo kutoka kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, na tayari imeundwa timu ambayo inapita kila eneo na kubaini namna gani nzuri ya kuweza kupeleka umeme na gharama nafuu katika maeneo hayo. Na katika bajeti tunayosoma kesho hilo ni eneo mojawapo ambalo tutalieleza na kutoa ahadi njema ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa leo tumeambiwa tarehe ya utekelezaji wa mradi huo na kwa kuwa kabla ya hapo tuliahidiwa kwamba mwezi wa Tatu mradi huu ungekuwa tayari.

Je, wananchi wa Vijiji hivyo kwenye Wilaya ya Rungwe wategemee kauli gani ya Serikali ya kuhakikisha hili jambo linakamilika kwa uweli baada ya miezi mitatu?

Mheshimiwa Naibu Spika, pili; Kijiji cha Ikombe Wilayani Kyela kilishafanyiwa uhakiki na kuwekea peg lakini mpaka sasa hivi hakuna dalili zozote za kupelekewa umeme wa REA: Je, ni lini Serikali itapeleka umeme huko?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Ally Jumbe kwa niaba ya Mheshimiwa Mwantona, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la kwanza ni kweli kwamba tulitarajia kumaliza mradi huu mapema lakini kama mnavyofahamu kulitokea ongezeko na mabadiliko makubwa sana ya bei na hivyo hata baada ya ukamilishaji wa kuangalia upungufu uliokuwa umejitokeza, tumeingia katika negotiation ya kuhakikisha kwamba tunapata fedha halisi ya kuweza kuongeza ili tumalize mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nawaahidi wananchi wa maeneo hayo kwamba baada ya kukamilisha mchakato wa kukubaliana bei halisi ya ongezeko la vifaa, sasa tupo tayari kwenda kupeleka umeme katika maeneo hayo kwa kurekebisha yale maeneo ambayo yalikuwa yamebakia.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika swali la pili. Katika kijiji hicho ambacho kimesemwa na vijiji vingine vyote ambavyo vipo Tanzania bara kama tulivyosema, vitapelekewa umeme kufikia Desemba mwaka huu kama ahadi ya Mheshimiwa Rais kwenye Ilani ilivyotolewa.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Kutokana na matatizo mbalimbali wanayopata wananchi wanaotumia umeme nje ya Gridi ya Taifa, mwezi wa Pili mwaka huu Wizara iliunda timu ya wataalam ikiongozwa na Mheshimiwa Naibu Waziri kuzungukia maeneo haya kusikiliza wananchi na baadaye kutoa uelekeo nini utatuzi wa changamoto zile, lakini tokea wakati huo mpaka sasa Wizara imekuwa kimya. Wananchi, wakiwemo wananchi wa Jimbo la Ukerewe Visiwa vya Gana na Ukara wanataka kusikia nini maelekezo na uelekeo wa Serikali juu ya changamoto hizi? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mkundi, Mbunge wa Ukerewe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli mimi mwenyewe nilifika Nansio, Ukerewe; nilifika Ukara, Gana, Kamasi, Irugwa katika visiwa vyote vya Ukerewe ili kuangalia changamoto ambayo wananchi wanaipata. Maeneo haya yapo mengi zaidi. Yalikuwepo mengine katika Mkoa wa Kagera na mengine katika maeneo ya Buchosa. Zoezi lile linaendelea na tunatarajia litakamilika mwishoni mwa mwezi huu. Litakapokuwa limekamilika, taarifa ya Serikali na maelekezo ya Serikali yatatolewa kwa maeneo yote ambayo yalikuwa na changamoto ya bei ya umeme na wananchi wataendelea kupata umeme kwa gharama ambazo ni nafuu ili Serikali iweze kuwahudumia vizuri.
MHE. EDWIN E. SWALLE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi. Jimbo la Lupembe katika Vijiji vya Lyalalo, Mfiriga, Itambo, Madeke na Kanikelele wamepata umeme wa REA, lakini tangu mwaka 2021 zimewekwa nguzo na hakuna ambacho kinaendelea. Wananchi hawa wangependa kujua nini mpango wa Serikali kufunga umeme hayo maeneo ambayo wananchi wangu wana nguzo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Swalle, Mbunge wa Lupembe kama ufuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tulivyosema hapo awali, kulitokea mabadiliko makubwa sana ya vifaa vya dukani hasa vinavyotengenezwa kwa kutumia chuma, alminium na Copper. Tumemaliza mazungumzo sasa ya kuona gharama ambazo zimeongezeka na Serikali inayo fedha ya kuongeza katika utekelezaji wa mradi huu, kutoka ile Shilingi trilioni 1,250.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika muda mfupi ujao wakandarasi watarudi site wakiwa sasa wamepata fedha ya nyongeza ya kununua vile vifaa ambavyo gharama zake zilikuwa zimepanda na mradi utaendelea kama uvyoanza na plan ilivyo.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwa kuwa kwenye mradi wa scope hii ya mwisho ya round III ya REA tuliongeza proposal ya kuongeza vijiji, hamlets na institutions, tukaipeleka REA na TANESCO kwa ajili ya utekelezaji, lakini tuliruka chanzo cha maji cha Kijiji cha Njomlole:-

Je,Serikali inaweza ikatuorodheshea Kijiji hicho pia ambacho kilirukwa kwa bajati mbaya ili kiingie katika mradi utakaokuja kwa vijiji tulivyoomba viongezwe na miradi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Vita Kawawa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ni eneo la kijiji, vijiji vyote vimechukuliwa na vipo kwenye mpango wetu wa REA III round II na umeme utafika katika eneo hilo. Ila nimesikia kwamba ni kwenye chanzo cha maji; upo mradi mahususi wa kupeleka umeme kwenye vyanzo vya maji, kwenye migodi na kwenye vituo vya afya. Tunazo site zaidi ya 560 ambazo zimechukuliwa katika bajeti inayokuja, tutaiweka eneo hilo kuwa mojawapo la kupelekewa umeme ili wananchi waweze kuendelea kupata huduma. (Makofi)

MHE. ZAYTUN S. SWAI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi hii. Wilaya ya Arumeru Mkoani Arusha ina changamoto kubwa sana ya kukamilika kwa miradi ya REA hususan kwenye Kata za Bangata, Oltroto na Lengijave; na hii imetokana na kubadilishwa kwa wakandarasi: -

Je, Serikali itatatua vipi changamoto hii?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Zaytun Swai, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, huko nyuma tulikuwa tuna utaratibu wa kutekeleza mradi uliokuwa unaitwa GOODS. Tunampa makandarasi fedha, anakwenda ananunua vifaa; kwenye mkataba unakuta asilimia 80 ni vifaa, asilimia 20 ndiyo labour. Akishanunua vifaa akapata faida yake, anaondoka, anatelekeza mradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huu tunaoutekeleza sasa, tumebadilisha utaratibu. Tunafanya kwa utaratibu unaoitwa WORKS. Tunamlipa mkandarasi kulingana na kazi aliyoifanya. Hatutarajii kuwepo na utelekezaji wa miradi wala kushindwa kukamilika kwa miradi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile hiyo ya nyuma, tumeongeza usimamizi. Kama mnavyofahamu, wasimamizi tangu ngazi ya Jimbo kuja kwenye Mikoa tunahakikisha kwamba miradi yote inakamilika kwa kadri tulivyojipangia.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa Mkoa wa Kigoma tulichelewa kupata umeme wa awamu ya kwanza na ya pili: Je, katika awamu wa tatu mzunguko wa pili, Serikali ipo tayari kumsimamia mkandarasi ili umeme uweze kufika vijijini na katika vitongoji vyote? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kauli ya Serikali na ahadi ya Serikali ni kusimamia wakandarasi bega kwa bega kuhakikisha kwamba miradi yote inakamilika kwa wakati na kwa kadri tulivyojipangia. Usimamizi huu ni wa vitendo; wapo wasimamizi kwenye ngazi za Jimbo wanakuja, wapo wasimamizi kwenye Kanda, wapo wasimamizi ngazi ya Taifa, na watu wote wamewezeshwa kuhakikisha kwamba kazi hizi zinafanyika na kukamilika kwa wakati.
MHE. SALMA R. KIKWETE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Nataka kujua tu kujua kuhusiana na suala la REA Awamu ya III ujazilizi. Kwenye Jimbo langu la Mchinga, nilibakiza vijiji 12. Naipongeza Serikali wamenipatia, lakini sambamba na hilo, kuna nguzo zimewekwa, sasa ni zaidi ya miezi sita hakuna kinachoendelea. Nini kauli ya Serikali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Salma Kikwete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunakiri kwamba tulipata changamoto kidogo ya miradi kutoendelea kwa kasi na speed tuliyoitarajia kwa sababu ya mabadiliko ya bidhaa za viwandani. Tunasema kwamba nguzo zilipatikana kirahisi, ni kwa sababu tulipolipa ile advace payment asilimia 20, Wakandarasi walitumia asilimia 15 kwenda kununua vifaa ambavyo vinapatikana hapa hapa nyumbani zikiwemo na nguzo. Kuja kuingia kwenye awamu ya pili ya kununua vifaa ambavyo vinatoka madukani, ndiyo sasa bei zimepanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, baada ya mazungumzo na committment ya Serikali ya kuongeza fedha, matatizo yote haya ya nguzo zilizosimama bila kuwekewa nyaya na transforma, zinaenda kwisha na kazi itaendelea kwa kasi kubwa zaidi. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa kuwa mpango wa REA kwa Mkoa wa Singida mpaka mwezi wa Saba wanatakiwa wawe wameunganisha vijiji 10 na umeme, lakini katika Wilaya ya Ikungi Majimbo ya Singida Magharibi na Mashariki vijiji saba vyote ni vya Jimbo la Singida Mashariki: -

Je, ni nini mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba wanaongeza idadi ya vijiji katika Jimbo la Singida Magharibi kutoka vitatu na kuendelea ili wananchi wapate huduma ya umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat Hanje, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii tunayoitekeleza inalenga kupeleka huduma kwa wananchi. Kwa hiyo, kama kijiji kimepata umeme kwenye mradi mmoja, kwa mfano vijiji alivyovisema saba vimepata umeme kutoka kwenye mradi wa backborn wa Mradi wa msongo wa kilovolt 400 kwenda Namanga, then vimeshapata umeme. Vile vijiji vingine vyote vilivyobaki ndiyo vinaingizwa kwenye REA III round II. Nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba hakuna kijiji hata kimoja kitakachobaki bila kupata umeme; kama hakipo kwenye REA III basi kitakuwa kipo kwenye mradi mwingine kwa ajili ya kpatiwa umeme. (Makofi)
MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mbulu Vijijini kuna kata tatu ambazo hazina umeme na vijiji 15. Nakubali majibu ya Mheshimiwa Waziri kwamba REA wameondoka site kutokana kupanda umeme na kupanda gharama za umeme: -

Je, ni lini mnamaliza huo utaratibu wa kukubaliana na hao wakandarasi ili warudi site wakakamilishe mradi huu wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Flatei, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi mwenyewe nilienda katika Jimbo lake kuzindua umeme katika REA III round II na kazi ilikuwa inaendelea. Kama alivyosema, ni kweli tulikuwa na changamoto hiyo, lakini tayari tumeshakamilisha taratibu za mazungumzo, na wakati wa maonesho hapa Mheshimiwa Waziri aliwaambia wakandarasi wote Serikali tayari imeshatoa fedha kwa ajili ya kuongeza ile nakisi iliyokuwepo. Kwa hiyo, wakandarasi wanarudi site kwa ajili ya kuendelea kufanya kazi wakiwa na uhakika kwamba Serikali ya Awamu ya Sita itatoa fedha ili kazi iweze kukamilika.
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Wilaya ya Kyerwa ina vijiji 29 ambavyo bado havijapatiwa umeme ikiwemo Kata ya Nkwenda Kijiji cha Kakerere, Kata ya Kakanja Kijiji cha Keshanda na Kata ya Lukolaijo Kijiji cha Mgorogoro. Navitaja hivi kwa sababu vipo mjini. Ni lini hivyo vijiji vitapatiwa umeme? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Anatropia, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni committment na Serikali kwamba itakapofika Desemba mwaka huu vijiji vyote viwe vimepelekewa umeme mabadiliko na nyongeza kidogo itatokana na changamoto ambazo wakati tunawasilisha bajeti tulizisema. Ila Kyerwa ni eneo mojawapo ambalo mkandarasi yupo site na kazi zinaendelea na tunaamini kwamba kazi itakamilika kwa jinsi tulivyojipangia. (Makofi)
MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Namshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la kwanza: Kwa kuwa ujenzi wa kituo hiki cha umeme umesimama kuanzia mwezi wa Tano mwaka 2022, na kwa taarifa tuliyonayo ni kwamba nguzo zitakazotumika ni za zege: Je, kwanini Serikali isitumie zile nguzo ambazo zimetupwa tangu mwaka 2020 mwezi wa Tano, zitumike kueneza au kusambaza umeme katika maeneo mengine kuliko kuachwa kama zilivyo porini na hata pengine kuzihatarisha na moto na kadhalika? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, wananchi ambao nguzo hizo za zege zitakazopita wanadai fidia; je, ni lini wananchi hawa watalipwa ili na wenyewe wajiendeleze kiuchumi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Margaret Sitta kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba design ya awali ilikuwa inatumia nguzo za miti, lakini baada ya maboresho imeonekana ni vema kubadilisha design hiyo na hivyo tutatumia nguzo nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu nimwambie Mheshimiwa Margaret, hizi nguzo tutazitumia kwa kadri ya mahitaji. Vile vile nguzo za kupeleka umeme zinatofautiana kulingana na mahitaji. Zile tulizopeleka kule ni za kupeleka msongo mkubwa wa kilovoti 132, ziko zile za msongo wa kilovoti 33 na ziko zile za distribution za kwenye maeneo yetu ya msongo wa kilovoti 400. Kwa hiyo hizi zilizoko kule tukizipeleka kusafirisha na kusambaza umeme kwa wananchi, tutakuwa tunatumia resource kubwa katika maeneo ambayo siyo yenyewe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tutapata nguzo nyingine kwa ajili ya kuwapelekea wananchi na hizi zitafanya kazi katika maeneo mengine ambapo zinatakiwa kufanya kazi bila kuathiri mahitaji yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye swali la pili, nadhani wiki hii kabla haijaisha, wale wataalam ambao walikuwa wanafanya survey kwa ajili ya kulipa compansation, wataanza kuonyesha yale majedwali ya wale wanufaika wa compansation kwa wananchi ili waweze ku-verify na kuona kama ndiyo stahiki na baada ya hapo sasa itarudishwa Wizarani kwa Mthamini Mkuu wa Serikali kwa ajili ya kusainiwa na kurekebisha upungufu utakaojitokeza. Tunaamini kwamba katika muda mfupi ujao wa mwezi mmoja au miwili basi fidia zitaanza kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Margaret Sitta awaambie wananchi wawe tayari, wiki hii au mwanzoni mwa wiki inayokuja kwenda kukagua zile fidia ambazo wameandaliwa kwa ajili ya kuhakiki ubora wake.
MHE. STANSLAUS S. MABULA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Naomba nimwulize Mheshimiwa Waziri kwamba mradi wa umeme jazilizi kwa kiasi kikubwa sana umefanikiwa, lakini kuna changamoto za upatikanaji wa fedha ili kukamilisha maeneo mengi zikiwemo Kata za Rwanima, Mahina Fumagila pamoja na Kishiri.

Ni lini sasa mkakati wa Serikali kuhakikisha fedha nyingi zinapatikana ili mradi jazilizi uoneshe maana halisi ya kujaziliza kwenye maeneo ambayo hayajapata umeme mpaka leo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mabula, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kaka yangu Mheshimiwa Mabula ananufaika na mradi unaoitwa Peri-urban ambao unapeleka umeme katika maeneo ya miji lakini yenye asili ya vijiji. Katika mwaka wa fedha unaokuja imetengwa pesa na eneo lake ni mojawapo ambalo litapelekewa umeme wa kuongezea kwenye yale maeneo ambayo bado hayajapatiwa umeme. Nimwahidi tu kwamba Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan imejikimu na kuamua kupeleka umeme katika kila eneo na pesa imetengwa ya kuanzia itapatikana katika mwaka huu wa fedha unaokuja, na muda sio mrefu ataona wakandarasi wakiwa site. Pia ziko jitihada za ziada za kuendelea kutafuta pesa kwa ajili ya kufikisha kwenye maeneo yote ambayo tunayo.
MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuuliza swali dogo la nyongeza kwamba Halmashauri ya Arusha DC inadai fidia ya umeme wa line kubwa inayokwenda Namanga, ni lini sasa Serikali itakamilisha ahadi hii, kwa sababu Halmashauri nyingine zote zimelipwa, imebaki tu Halmashauri Arusha DC?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Lemburis Noah Saputi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba mradi mkubwa anaosema ulikuwa unatoa umeme Iringa kupita Dodoma - Singida kwenda Arusha mpaka Namanga, na kuna maeneo ambayo tayari fidia ilishafanyika. Yalibakia yale maeneo machache ambayo yalikuwa yana matatizo na kutoeleweka kwa nani alipwe fidia au pengine fidia ilitakiwa ilipwe Serikali, wamepewa maeneo mbadala ili wajengewe majengo. Jambo hili tumekubaliana Wizarani kwamba kabla mwaka huu haujaisha, basi yale maeneo ambayo tayari fidia zilishaanza kulipwa yakamilike na pale ambapo pana changamoto kubwa, tujue namna ya kuitatua.

Kwa hiyo, namwahidi kwamba jambo hili tunalifanyia kazi na tutalikamilisha katika muda mfupi ujao.