Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to Primary Questions by Hon. Stephen Lujwahuka Byabato (116 total)

MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali italipa fidia kwa Wananchi wa Kibaha Mjini ambao maeneo yao yalitwaliwa kwa ajili ya mradi wa umeme wa Msongo wa KV 400 kutoka Kinyerezi hadi Arusha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa makofi hayo yanaashiria nyota njema.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa, basi nichukue nafasi fupi kuwashukuru wanachama wa Chama cha Mapinduzi lakini nikishukuru Chama changu cha Mapinduzi, niwashukuru wana Jimbo la Bukoba Mjini na nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kunipa nafasi hii ya kutekeleza kipande hiki cha majukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvetry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kazi ya uthamini wa mali za wananchi katika mradi wa ujenzi wa njia za kusafirisha umeme kilovoti 400 kutoka Kinyerezi kupitia Kisarawe, Kibaha hadi Chalinze ilifanyika kati ya mwaka 2015 na 2016 ili kuwezesha pamoja na mambo mengine wananchi wanaopitiwa na mradi kulipwa fidia na kupisha ujenzi wa mradi huo. Taratibu zote za uandaaji wa taarifa na majedwali ya fidia zilikamilika mwezi Machi 2020. Fidia kwa ajili ya maeneo kati ya Kiluvya (Kisarawe) hadi Chalinze ni takriban shilingi bilioni 21.569.

Mheshimiwa Spika, aidha, malipo haya yanahusisha Halmashauri za Kisarawe, Kibaha Mjini, Kibaha Vijijini na Chalinze. Kwa sasa taratibu za kuhamisha fedha za fidia kutoka Wizara ya Fedha na Mipango kwenda TANESCO ili kuwalipa fidia wananchi hao zinaendelea. Fidia ya wananchi hao italipwa mara tu baada ya taratibu hizo kukamilika.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wa Wilaya za Ilala, Ubungo, Kisarawe, Kibaha na maeneo ya Chalinze waliopisha mradi huo kuwa na subira wakati Serikali inakamilisha taratibu za malipo ya fidia kwa wananchi hao.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA aliuliza:-

Je, ni lini mradi wa kujenga Sub-station ya Nyakanazi (KV 220) toka Rusumo na Geita utakamilika ili kuondoa tatizo la kukatikakatika kwa umeme Biharamulo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Wizara ya Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) linatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovolti 220 kutoka Geita hadi Nyakanazi. Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 220 kutoka Geita - Nyakanazi yenye urefu wa kilometa 144 ambapo Mkandarasi Kampuni ya M/S Kalpataru Power Transmission Ltd kutoka nchini India anaendelea na kazi za mradi. Hadi sasa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme pamoja na kituo cha kupoza umeme umefikia asilimia 60.

Mheshimiwa Spika, gharama ya mradi ni EURO milioni 45 sawa na takriban shilingi bilioni 117.79. Mradi huu unatarajiwa kukamilika Machi, 2021. Ni mategemeo ya Serikali kuwa mradi utakapokamilika utaimarisha na kuboresha hali ya upatikanaji umeme katika maeneo ya Wilaya ya Biharamuro na maeneo mengine ya jirani.
MHE. SHABANI O. SHEKILINDI Aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuvipatia umeme vijiji 32 vya Jimbo la Lushoto ambavyo havina umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Shabani Omari Shekilindi, Mbunge wa Lushoto na tabibu wetu humu ndani, kwa wale ambao tunaamini kikombe, kama ifuatavyo:- (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza miradi ya kusambaza umeme vijijini kwa awamu kadri ya upatikanaji wa fedha. Malengo ya Serikali ni kufikisha umeme katika vijiji vyote vya Tanzania Bara ifikapo Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali iko katika hatua za mwisho kukamilisha maandalizi ya ujenzi wa mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu mzunguko wa pili (REA III round two). Kwa Wilaya ya Lushoto Mradi wa REA III mzunguko wa pili unapeleka umeme katika maeneo ya vijiji vyote 32 vya Jimbo la Lushoto ambavyo havikupata umeme kupitia miradi ya kusambaza umeme ya awamu ya pili na awamu ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi ya kusambaza umeme kwa Wilaya ya Lushoto zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa kilovoti 33; urefu wa kilomita 131.8; njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 umbali wa kilomita 381.9; ufungaji wa transfoma 99 za 50kVA; pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,984. Mradi unakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 16.8. Utekelezaji wa mradi utaanza Februari, 2021 na kukamilika ifikapo Desemba, 2022.
MHE. AUGUSTINE V. HOLLE Aliuliza: -

Je, ni lini Mkoa wa Kigoma utaunganishwa na umeme wa Gridi ya Taifa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Augustine Vuma Holle, Mbunge wa Kasulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kigoma unapata umeme kupitia mitambo ya kuzalisha umeme kwa kutumia mafuta ya diesel ambayo ni gharama kubwa kwa TANESCO na Serikali kwa ujumla. Katika hatua ya haraka, Serikali inatekeleza mradi wa kuunganisha Mkoa wa Kigoma katika Gridi ya Taifa kutoka Tabora.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu utahusisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Kigoma kupitia Urambo na Nguruka umbali wa kilomita 395, pamoja na ujenzi wa vituo vya kupozea umeme wa msongo wa kilovoti 132 kwenda 33 vya Urambo, Nguruka na Kidahwe Mkoani Kigoma. Gharama za mradi huu ni shilingi bilioni 142.7 na mradi ulianza ujenzi mwezi Juni, 2020 na unatarajia kukamilika mwezi Juni, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine Serikali inaendelea na utekelezaji wa mradi wa ujenzi wa njia kuu za kusafirisha umeme, msongo wa kilovoti 400 yenye urefu wa kilomita 280 ya kutoka Nyakanazi Mkoa Kagera hadi Kidahwe Mkoani Kigoma. Mradi huu unahusisha ujenzi wa vituo viwili vya kupoza umeme msongo wa kilovoti 400 kuja 220 kwenda 132 mpaka 33 na 400/132/33 vya Nyakanazi vyenye transfoma mbili zenye ukubwa wa MVA 120.

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa mradi huu pia ulianza mwezi Januari mwaka 2020 na utakamilika mwezi Juni, 2022. Gharama ya mradi ni dola za Kimarekani milioni 187 chini ya ufadhili wa Serikali ya Tanzania, Benki ya Maendeleo ya AfDB pamoja na Benki ya Maendeleo ya Korea.
MHE. JOSEPH M. MKUNDI Aliuliza: -

Pamoja na kazi kubwa iliyofanywa na Serikali ya kusambaza umeme vijijini kupitia Mradi wa REA bado kuna shida kubwa katika maeneo ya vitongoji kwenye vijiji hivyo.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuwa umeme unasogezwa kwenye maeneo ya vitongoji ambavyo havijapata huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi, Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kutekeleza mradi wa kusambaza umeme katika vitongoji visivyokuwa na umeme kupitia mzunguko wa pili wa mradi jazilizi (Densification IIA) katika mikoa tisa ya Mbeya, Pwani, Tanga, Kilimanjaro, Dodoma, Singida, Tabora, Shinyanga na Mwanza kwa kupeleka umeme katika vitongoji 1,103 kwa kuunganisha umeme wateja wa awali wapatao 69,079. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 197. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2021. Kazi hii ni endelevu inayofanyika pia kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO).

Mheshimiwa Spika, ili kutimiza Azma ya Serikali ya kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji, Serikali kupitia Mradi wa Densification IIB unaotarajiwa kuanza mwezi Aprili, 2021 utaendelea kupeleka umeme katika vitongoji vya mikoa kumi ya Arusha, Geita, Kagera, Katavi, Kigoma, Lindi, Morogoro, Njombe, Simiyu, Songwe, kwa kupeleka umeme katika vitongoji 1,686 na kuunganisha umeme wateja wa awali wapatao 95,334. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 230. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2022.
MHE. VENANT D. PROTAS Aliuliza:-

Jimbo la Igalula lina jumla ya vijiji 58, ambapo Vijiji 12 vimepata umeme na vijiji 46 bado havijapata umeme:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme katika vijiji 46 ambavyo havijapata umeme?

(b) Je, gharama za kuunganisha umeme kwa kila mwananchi ni kiasi gani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daud Protas Venant, Mbunge wa Igalula, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vilivyobaki 46 katika Jimbo la Igalula vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya III mzunguko wa pili unaoanza katikati ya mwezi Februari 2021. Mradi huu utatekelezwa kwa kipindi cha miezi 18 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Septemba, 2022. Kukamilika kwa utekelezaji wa mradi huo, kutafanya vijiji vyote katika Jimbo la Igalula kupatiwa umeme.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua ya kuongeza kasi ya kutoa huduma ya umeme nchini mwaka 2019, Serikali kupitia TANESCO ilipunguza bei ya kuunganisha huduma ya umeme kwa wananchi wanaoishi vijijini na maeneo yanayofanana na hayo kutoka wastani wa shilingi 725,000/= kwa mita za njia tatu (three phase) hadi shilingi 139,000/= ikiwa ni punguzo la asilimia 80. Vilevile kwa mita za njia moja (single phase) kutoka wastani wa shilingi shilingi 177,000/= hadi shilingi 27,000/= sawa na punguzo la asilimia
84.75. Kwa ujumla, gharama hizo ni tozo ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT).
MHE. DKT. OSCAR I. KIKOYO Aliuliza:-

Ofisi ya TANESCO Wilaya ya Muleba inazidiwa na wingi wa wateja kutokana na miradi ya REA.

Je, ni lini Wilaya hiyo itapewa hadhi ya Mkoa wa TANESCO ili iweze kutoa huduma kwa wakati?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Oscar Ishengoma Kikoyo, Mbunge wa Muleba Kusini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Umeme nchini (TANESCO) limekuwa likiweka ofisi za Mikoa katika maeneo mbalimbali kwa kuzingatia vigezo mbalimbali ikiwa ni pamoja na ongezeko la shughuli za kiutendaji za Shirika na mahitaji ya umeme pamoja na wateja.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kusogeza huduma kwa wateja karibu Wilayani Muleba, TANESCO imefungua ofisi ndogo (sub-office) eneo la Kamachumu na imeshaanza kutoa huduma kwa wateja wa Kamachumu katika Jimbo la Muleba Kaskazini na maeneo mengine ya jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, TANESCO inatarajia kufungua ofisi ndogo (sub-office) nyingine eneo la Kyamyorwa na Bulyage ili kusogeza karibu zaidi huduma kwa wateja wa maeneo hayo na jirani. Ofisi hizo zitakuwa na wafanyakazi pamoja na vitendea kazi vyote vinavyohitajika ikiwa ni pamoja na usafiri.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA Aliuliza:-

(a) Je, ni kwa nini vijiji vyote vya Wilaya ya Kakonko havijapata umeme?

(b) Je, ni lini vijiji hivyo vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Buyungu, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Buyungu lina jumla ya vijiji 44, vijiji 40 tayari vinapatiwa umeme kupitia awamu ya pili na ya tatu ya utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini. Kazi inayoendelea sasa ni kuunganisha umeme katika vijiji 22 kwa wateja ambavyo vilipata umeme tayari ili kukamilisha mpango kazi aliyopewa mkandarasi katika eneo hilo. Kazi hiyo, inatarajia kukamilika ifikapo mwezi Aprili, 2021.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa usambazaji wa umeme vijijini umekuwa unafanyika kwa awamu, vijiji vinne vilivyobaki ambavyo ni Kijiji vya Rumashi, Nyamtukuza, Nyabibuye na Kinyinya viko katika mpango wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili utakaoanza mwezi Februari 2021 na kukamilika Septemba, 2022.
MHE. VITA R. KAWAWA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza umeme wa REA kwenye baadhi ya vitongoji vya vijiji vya Namtumbo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vita Rashid Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) pamoja na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme katika vijiji na vitongoji nchini. Vijiji vyote 14 vilivyobaki katika Wilaya ya Namtumnbo vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaotarajiwa kuanza mwezi Februari, 2021 na kukamilika mwezi Septemba, 2022. Mradi huu utahusisha pia kupelekea umeme vitongoji vya vijiji vitakavyopelekewa umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuliarifu Bunge lako tukufu kuwa vitongoji vyote nchini vikiwemo vya Wilaya ya Namtumbo vitaendelea kupelekewa umeme kupitia miradi ya umeme vijijini kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. REUBEN N. KWAGILWA Aliuliza:-

Je, ni lini wananchi katika mitaa 30 isiyo na umeme Wilayani Handenni watapatiwa umeme kulipia mradi wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Reubne Nhamanilo Kwagilwa Mbunge wa Handeni kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kutekeleza mradi wa kusambaza umeme katika vijiji, mitaa na vitongoji visivyokuwa na umeme kupiitia miradi mbalimbali. Kwa sasa mkandarasi Kampuni ya M/S Sengerema Engineering Ltd. amepewa kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 15 na mitaa vitongoji zaidi ya 30 katika Wilaya ya Handeni.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi hizo zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme wa msongo wa KV 0.4 umbali wa km. 27.5, ufungaji wa transfoma 11 za 50 kVA na 100 kVA; pamoja na kuwaunganisha wateja wa awali 669. Mradi unakadiriwa kugharimu shilingi bilioni 3.36. Utekelezaji wa mradi umeanza mwezi Februari, 2020 na utakamilika ifikapo Disemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, TANESCO inaendelea kuunganisha umeme kwa wateja ambao hawajaunganishiwa umeme katika mitaa na vitongoji vya Tanzania Bara ikiwemo Wilaya ya Handeni kupitia majukumu yake ya kila siku.
MHE. JUMANNE A. SAGINI Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itazipatia umeme kaya na vitongoji ambavyo havijapatiwa umeme Wilayani Butiama?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jumanne Abdallah Sagini, Mbunge wa Butiama, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kutekeleza mradi wa kupeleka umeme katika mitaa na vitongoji ambavyo havijapata umeme ikiwemo Wilaya ya Butiama. Serikali imeanza maandalizi ya kutekeleza mradi unaohusishwa ujenzi wa miundombinu ya umeme ya njia ya msongo wa kilovoti 0.4 zenye urefu wa kilometa 1,620, ufungwaji transforma 648 na kuunganisha wateja wa awali 48,600 katika vitongoji 648 nchini ikiwa ni pamoja na kaya na vitongoji vya Wilaya ya Butiama ambavyo havijapata umeme. Gharama ya mradi huuni shilingi bilioni 75. Ujenzi wa mradi huu unatarajiwa kuanza julai, 2021 na kukamilika mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa utekelezaji wa mradi huu kutatimiza azma ya Serikali ya kufikisha huduma ya umeme katika vitongoji vyote vya Wilaya ya Butiama.
MHE. KUNTI Y. MAJALA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itasambaza umeme katika Kata za Handa, Lalta, Sanzawa na Mpendo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunti Yussuf Majala, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji ambavyo havijapata umeme katika Wilaya ya Chemba vikiwemo vijiji vya Kata za Handa, Lalta, Sanzawa na Mpendo vitapatiwa umeme kupitia mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa pili ulioanza kutekelezwa mwezi Machi, 2021 na utekelezaji wa mradi huu utakamilika ifikapo Desemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi za mradi kwa Wilaya ya Chemba zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 umbali wa kilomita 681.4, msongo wa kilovoti 0.4 umbali wa kilomita 50, ufungaji wa transfoma 50 za 50kVA, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali wapatao 1,100 kwa gharama ya takriban Shilingi Bilioni 27.3.
MHE. ABDALLAH J. CHAUREMBO Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza transfoma ya 100 MVA katika substation ya Mbagala ili kuondoa tatizo la kukatika umeme katika Jimbo la Mbagala?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abdallah Jafari Chaurembo, Mbunge Wa Mbagala, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa kituo cha kupoza umeme cha Mbagala msongo wa kilovoti 132/33 chenye uwezo wa MVA 50 ulikamilika na kuanza kufanya kazi rasmi tarehe 25 Februari 2018, kupitia utekelezaji wa mradi wa TEDAP chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia. Baada ya kituo hiki kuanza kufanya kazi, hali ya upatikanaji umeme katika eneo la Mbagala uliimarika ikilinganishwa na kipindi cha nyuma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kukamilika kwa ujenzi wa kituo hicho cha kupoza umeme, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi wa kuboresha vituo vya kupoza umeme vya Kinyerezi na Mbagala kwa kufunga transfoma zenye uwezo wa MVA 50 kwa kila kituo pamoja na kuongeza uwezo wa njia ya kusafirisha umeme ya kilovoti 132 kutoka Kinyerezi hadi Mbagala kupitia Gongo la Mboto. Mradi huu unatarajia kutekelezwa kwa kipindi cha miezi kumi kuanzia Juni, 2021 na kukamilika Aprili, 2022. Gharama ya mradi huu ni takriban Dola za Marekani milioni 9.

Mheshimiwa Naibu Spika, kukamilika kwa utekelezaji wa mradi huu, kutaboresha hali ya upatikanaji umeme katika maeneo ya Mbagala na maeneo mengine ya jirani yanayopatiwa umeme kutoka katika kituo hicho.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kusambaza umeme katika Vijiji na Vitongoji kupitia REA III hasa katika maeneo ambayo nguzo zimetelekezwa barabarani zaidi ya miaka miwili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zuena Athumani Bushiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini - REA na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO), inaendelea kutekeleza mpango wake wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu, mzunguko wa pili katika vijiji vyote nchini. Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Disemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa Mradi huu unalenga kufikisha umeme katika vijiji 1,956 kati ya vijiji 12,268 ambavyo havijafikiwa na umeme. Kazi ya kupeleka umeme katika vitongoji ni endelevu inayoendelea kutekelezwa kupitia TANESCO na REA ikiwa ni kazi ya kuendelea kuunganisha huduma ya umeme kwa wananchi.
MHE. DAIMU I. MPAKATE K.n.y. MHE. HASSAN Z. KUNGU Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Umeme Wilayani Tunduru chenye uwezo wa kupokea 132 KV ambazo ni uhitaji halisi kwa Wilaya ya Tunduru, Nanyumbu na Masasi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Tunduru Kaskazini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) inaendelea na upembuzi yakinifu kwa ajili ya kutekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovoti 132 kutoka Songea hadi Masasi kupitia Namtumbo, Tunduru na Nanyumbu umbali wa kilometa 395.

Mheshimiwa Naibu Spika, (TANESCO) pia inaendelea na taratibu za ujenzi wa Vituo vya kupoza umeme vya msongo wa kilovoti 132 kwenda 33 vya Namtumbo na Tunduru Mkoa wa Ruvuma, pamoja na vituo vya Nanyumbu na Masasi Mkoa wa Mtwara. Ujenzi wa mradi unatarajiwa kuanza ifikapo Desemba, 2022 na kukamilika mwezi Desemba, 2023 na gharama ya mradi inakadiriwa kuwa shilingi bilioni 132.7.
MHE. SAMWELI H. XADAY aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga kituo cha kupooza umeme Mjini Katesh kwani kuna line ndefu ya Km 780 hivyo kusababisha umeme kukatika mara kwa mara Wilayani Hanang?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI aljibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Samwel Hhayuma Xaday, Mbunge wa Hanang, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) limeanza taratibu za ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme pamoja na kituo kidogo (switching yard) cha kilovoti 33 kutoka njia kuu ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 inayoendelea kujengwa kutoka Singida hadi Namanga katika Kijiji cha Mogitu Wilayani Hanang.

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa kituo hicho utaboresha hali ya upatikanaji wa umeme katika maeneo ya Wilaya ya Hanang na maeneo jirani utaanza mwezi Julai, 2022 na kukamilika Juni, 2023. Gharama ya mradi ni takribani shilingi bilioni 2.6. Utekelezaji wa mradi huu utagharamiwa na Serikali kwa asilimia 100.
MHE. EDWARD O. KISAU aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa ajira za upendeleo kwa vijana na fursa nyingine za kibiashara kwa wananchi wa Jimbo la Kiteto kupitia mradi mkubwa wa kimkakati wa Bomba la Mafuta (Hoima – Tanga) ambalo linapita katika Wilaya ya Kiteto?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Edward Olelekaita Kisau, Mbunge wa Kiteto, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Uganda inatekeleza Mradi wa Ujenzi wa Bomba la Kusafirisha Mafuta Ghafi kutoka Kabaale/Hoima nchini Uganda hadi Chongoleani, Mkoani Tanga nchini Tanzania. Kwa upande wa Tanzania, bomba litapita katika Mikoa 8 na Wilaya 24 ambapo Wilaya ya Kiteto itapitiwa na bomba kwa urefu wa kilomita 117.1 pamoja na ujenzi wa kambi ya kuhifadhi mabomba katika kijiji cha Ndaleta na kambi ya wafanyakazi katika Kijiji cha Njoro.

Mheshimiwa Spika, kutokana na Bomba hilo kupita katika Wilaya ya Kiteto, wananchi wa Kiteto watanufaika na ujenzi wa mradi huu kwa kufanya biashara, ajira na fursa nyingine za kiuchumi na kijamii. Utekelezaji wa kazi za mradi huu unatarajiwa kuanza mwezi Julai, 2021 na kukamilika mwezi Julai, 2023.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Nishati kwa kushirikiana na wadau wengine inaendelea kutoa hamasa ili wananchi wanufaike na shughuli za ujenzi na uendeshaji wa mradi.
MHE. BONNAH L. KAMOLI K.n.y. MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia Wananchi wa Chalinze waliopisha ujenzi wa miundombinu ya miradi ya kusafirisha umeme kutoka Kinyerezi na Bwawa la Mwalimu Nyerere?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ridhiwani Jakaya Kikwete, Mbunge wa Chalinze, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inatekeleza mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Kituo cha Kuzalisha Umeme cha Mwalimu Julius Nyerere hadi Chalinze lakini pia ujenzi wa Kituo cha Kupoza Umeme katika Kijiji cha Chaua - Chalinze.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO imekamilisha tathimini ya mali za wananchi na Taasisi zilizopisha utekelezaji wa mradi huu na fidia kuidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali. Jumla ya shilingi bilioni 42.3 zimetengwa katika bajeti ya mwaka 2021/2022 kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi waliopisha mradi. Fidia ya wananchi hao itaanza kulipwa muda wowote kuanzia mwaka wa fedha 2021/2022 baada ya taratibu zote kukamilika.
MHE. DKT. JASSON S. RWEIKIZA aliuliza:-

Je, ni lini umeme utapelekwa katika Vijiji vya Buzi, Buguruka, Musina, Nsheshe na vingine ambavyo havijafikiwa na umeme katika Jimbo la Bukoba Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Jasson Samson Rweikiza, Mbunge wa Bukoba Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme na kufikisha katika vijiji vyote vya Tanzania Bara ifikapo Desemba, 2022. Vijiji vinane kati ya vijiji 94 vya Bukoba Vijijini ambavyo ni Kijiji cha Buzi, Buguruka, Musira, Nsheshe, Ngarama, Omubweya, Kagarama na Rukoma vinatarajiwa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ulianza kutekelezwa Mwezi Machi, 2021 na unatarajia kukamilika Mwezi Desemba, 2022 na gharama ya mradi huu kwa Jimbo la Bukoba Vijijini ni shilingi bilioni 2.04.
MHE. HUSNA J. SEKIBOKO - K.n.y. MHE. MWANTUMU M. ZODO aliuliza:-

Usambazaji wa umeme vijijini unapaswa kukamilika ifikapo Mwaka 2021/2022:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuwa usambazaji wa umeme vijijini unakamilika kama ilivyopangwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Mzamili Zodo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme (TANESCO) inaendelea kutekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili. Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Disemba, 2022. Mradi huu unalenga kufikisha umeme katika vijiji 1,974 ambavyo havijafikiwa na miundo mbinu ya umeme. Aidha, mradi huu pia, utafikisha umeme katika vitongoji 1,474.

Mradi huu utakapokamilika utafanya vijiji vyote 12,268 vya Tanzania Bara kufikiwa na miundo mbinu ya umeme na gharama ya mradi huu ni takribani shilingi 1,040,000,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha kuwa mradi huu unakamilika kwa wakati, Serikali imeweka mikakati mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuongeza usimamizi, kupunguza wigo wa kazi za wakandarasi ili kurahisisha usimamizi, wakandarasi kulipwa kwa wakati na kuhakikisha vifaa vyote vinavyohusika vinapatikana nchini.
MHE. JULIANA D. SHONZA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 127 vilivyobaki vya Mkoa wa Songwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Songwe una jumla ya vijiji 307 ambapo kati ya hivyo, vijiji 180 tayari vimeapatiwa umeme na vijiji 127 bado havijapatiwa umeme. Nia ya Serikali ni kuvipatia umeme vijiji vyote visivyo na umeme kabla ya mwisho wa mwaka 2022.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme katika vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na umeme Tanzania Bara. Vijiji 127 vilivyobaki katika Mkoa wa Songwe vitapatiwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ambapo utekelezaji wake ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi kwa Mkoa wa Songwe zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilomita 1,065.4, msongo wa kilovoti 0.4 urefu wa kilomita 120, ufungaji wa transfoma 120 za 50kVA, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 2,640. Gharama ya mradi huu ni takriban shilingi bilioni 38.7.
MHE. LEAH J. KOMANYA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Kata za Mwamalole, Mbushi, Mwamanongu, Imalaseko, Mwamanimba, Mwabuzo na Kimali ili wananchi waweze kufaidika na huduma hiyo na kuchochea maendeleo katika Kata hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Mradi Kabambe wa kupeleka umeme vijijini unaosimamiwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme katika kata na vijiji vyote ambavyo havijafikiwa na umeme Tanzania Bara zikiwemo Kata za Mwamamole, Mwamanimba, Mwabuzo, Imalaseko, Mwamanongu, Mbushi na Kimali. Kata hizi pamoja na vijiji vyake vyote vya Meatu vinatarajiwa kufikishiwa umeme ifikapo mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi katika Wilaya ya Meatu zinajumuisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 555.90, msongo wa kilovoti 0.4 urefu wa kilomita 48, ufungaji wa transfoma 48 za 50kVA, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali 1,056. Gharama ya mradi huu ni takriban shilingi bilioni 22.6.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatatua mgogoro wa bei ya umeme unaotumika na Watanzania waishio Zanzibar ili kuweka usawa kwa Watanzania wote?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ali Hassan Omar King, Mbunge wa Jang’ombe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar zimeendelea kushughulikia suala la bei ya kuuza na kununua umeme baina ya Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) ili kuupatia ufumbuzi mgogoro huo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha mwaka 2020/2021 Timu ya Wataalamu wa Taasisi husika zilikutana katika vikao mbalimbali na kufanya uchambuzi wa kina wa vigezo vilivyohusika katika kupanga bei hiyo ya kuuzia umeme kwa wateja wakubwa wa kununua umeme ikiwemo ZECO. Kutokana na uchambuzi huo, inapendekezwa kuwa vigezo hivyo vipitiwe upya ili kuleta unafuu kwa wateja wa aina hiyo ikiwemo ZECO.

Mheshimiwa Naibu Spika, mapendekezo hayo yaliwasilishwa katika Kamati ya Wizara zinazoshughulikia masuala ya Muungano ili kufanyia kazi mapendekezo hayo na kupata ufumbuzi wa kudumu wa suala hili.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA aliuliza: -

Je, ni lini Vijiji na Vitongoji nchini ambavyo havijapatiwa umeme vitapatiwa huduma hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deodatus Philip Mwanyika, Mbunge wa Njombe Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) na Shirika la Umeme nchini (TANESCO) inaendelea kutekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini Awamu ya III mzunguko wa pili. Mradi huu unatarajiwa kufikisha miundombinu ya umeme katika vijiji vyote 1,974 ambavyo havijapata umeme kati ya vijiji 12,268 vya Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, mradi huu pia utafikisha umeme katika vitongoji 1,474 ambavyo havijafikiwa na umeme. Mradi ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika ifikapo Desemba, 2022. Gharama ya mradi ni takriban bilioni 1,176.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vitongoji ni endelevu. Serikali kupitia REA na TANESCO itaendelea kupeleka umeme katika vitongoji vyote mwaka hadi mwaka kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. TUNZA I. MALAPO aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaunganisha mfumo wa gesi asilia kwa ajili ya kupata nishati ya kukaangia samaki katika Soko la Feri Manispaa ya Mtwara Mikindani?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tunza Issa Malapo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC) inaendelea na kazi ya ujenzi wa miundombinu ya kusambaza gesi asilia katika mikoa mbalimbali nchini ukiwemo Mkoa wa Mtwara kwa ajili ya matumizi ya viwandani, majumbani na taasisi za umma na binafsi. Katika Mkoa wa Mtwara, mradi huu unahusisha ujenzi wa miundombinu ya kusambaza gesi asilia kwa njia za mabomba na vituo vya kuongeza mgandamizo wa gesi (Compressed Natural Gas (CNG) Stations).

Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa miundombinu ya usambazaji wa gesi asilia katika Soko la Feri katika Manispaa ya Mtwara Mikindani upo katika hatua ya kukamilisha usanifu wa kina wa kihandisi, utakaofuatiwa na hatua ya kumpata mkandarasi wa ujenzi wa mradi huo. Kazi ya usanifu inatarajiwa kukamilika mwezi Agosti, 2021 na ujenzi kuanza Desemba, 2021 na kukamilika Juni, 2022. Gharama za mradi ni takribani shilingi bilioni 10.11.
MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA aliuliza:-

Umeme wa msongo mkubwa wa KV 400 toka Singida hadi Namanga umepita katika baadhi ya maeneo ya wazi na malisho ya mifugo 6 kwenye Vijiji vya Engikaret, Ranchi, Orbomba, Kimokouwa na Eorendeke; na fedha za fidia ilipendekezwa zitolewe kwa ajili ya Miradi ya Maendeleo ya Vijiji husika pamoja na watu binafsi ambao umeme huo umepita kwenye makazi yao:-

Je, ni lini fedha hizo zitatolewa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Steven Lemomo Kiruswa, Mbunge wa Longido, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la TANESCO inaendelea kukamilisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Singida hadi Namanga. Lengo kuu la mradi huu ni kuimarisha umeme katika Gridi ya Taifa na kuunganisha Tanzania na nchi za Zambia na Kenya katika gridi ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mradi huu mwezi Septemba, 2020 Serikali kupitia TANESCO ililipa fidia jumla ya shilingi bilioni 11.33 kwa wananchi wapatao 645 katika Wilaya ya Longido ikiwamo Vijiji vya Engikaret, Ranchi, Orbomba, Kimokouwa na Eorendeke. Malipo hayo yamelipwa kama ifuatavyo; Kijiji cha Eorendeke jumla ya shilingi 439,780,320, Kijiji cha Kimokouwa jumla ya shilingi 165,564,000, Kijiji cha Orbomba jumla ya shilingi 343,662,080 na Kijiji cha ranchi jumla ya shilingi 720,754,200.

Mheshimiwa Spika, malipo ya fedha hizi yalifanyika kwa njia ya hundi kupitia Ofisi ya Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Longido.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza:-

Je, Serikali ipo tayari kuanzisha Wilaya ya TANESCO kwa ajili ya kuhudumia viwanda na wananchi katika Mji wa Mafinga ili kuendana na kasi ya uchumi wa viwanda?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mufindi ina Halmashauri mbili ambazo ni Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi na Halmashauri ya Mji wa Mafinga. Katika Halmashauri ya Mji wa Mafinga, ipo Ofisi ya Wilaya ya TANESCO inayotoa huduma kwa wananchi wa Mji wa Mafinga pamoja na wananchi wa Wilaya ya Mufindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa, Ofisi ya TANESCO iliyopo Mafinga inakidhi mahitaji ya kutoa huduma kwa wananchi wote wa Mji wa Mafinga ikiwa ni pamoja na wateja wa viwanda vikubwa 80, wateja wa viwanda vidogo vidogo 445 na wateja wadogo 23,207. Hata hivyo, Serikali kwa kutambua ukuaji wa shughuli za kiuchumi katika Mji wa Mafinga, TANESCO imefungua Ofisi Ndogo (Sub Office) katika Kata ya Igowelo, Kibao na Mgololo katika Kata ya Makungu. Ofisi hizi zimeanzishwa ili kusogeza huduma karibu kwa wananchi walio mbali na Mji wa Mafinga ikiwa ni pamoja na kuhakikisha huduma zinatolewa kwa urahisi kwa wananchi wa maeneo hayo.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza:-

Je, ni lini wananchi wa Kata ya Ugalla watapatiwa umeme wa REA III?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na utekelezaji wa miradi ya kupeleka umeme vijijini kwa nchi nzima kwa kupeleka umeme katika vijiji ambavyo havijafikiwa na umeme.

Mheshimiwa Spika, vijiji tisa vya Jimbo la Nsimbo ambavyo havina umeme ikiwa ni pamoja na Vijiji vya Kata ya Ugalla vya Katambike, Mnyamasi na Kasisi vitapatiwa umeme kupitia Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu mzunguko wa pili unaoendelea. Utekelezaji wa mradi huu ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo inahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33, urefu wa kilomita 63.6; msongo wa kilovoti 0.4, urefu wa kilomita 3.0; na ufungwaji wa transfoma tatu, pamoja na kuwaunganishia umeme wateja wa awali zaidi ya 66. Gharama ya mradi ni Shilingi bilioni 2.46.
MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE aliuliza:-

Je, ni lini ujenzi wa Mradi wa Umeme wa Maji kutoka Mto Rumakali katika Kata ya Lufilyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Atupele Fredy Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme nchini (TANESCO) inatekeleza Mradi wa Kuzalisha Umeme kwa kutumia maporomoko ya maji ya Mto Rumakali, Mkoani Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi huu unahusu ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme cha megawati 222 na njia ya kusafirisha umeme msongo wa kilovoti 220 yenye urefu wa kilomita 150 kutoka Rumakali hadi Kituo cha Kupoza Umeme cha Iganjo, Mkoani Mbeya. Gharama za mradi ni takriban shilingi bilioni 913.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatua iliyofikiwa sasa ni kukamilisha taratibu za manunuzi ya Mkandarasi wa ujenzi wa mradi. Kazi za ujenzi zinatarajiwa kuanza mwezi Oktoba, 2021 na kukamilika mwezi Juni, 2024.
MHE. MIRAJI J. MTATURU aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itafikisha umeme katika vijiji 28 ambavyo bado havijapata umeme kati ya vijiji 50 vya Jimbo la Singida Mashariki?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Miraji Jumanne Mtaturu, Mbunge wa Singida Mashariki, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme vijijini na kuufikisha katika vijiji vyote vya Tanzania Bara ifikapo mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Singida Mashariki lina jumla ya vijiji 50. Vijiji 22 tayari vina umeme; vijiji 12 vinapatiwa umeme sasa kupitia Mradi wa Ujazilizi (Densification) ulioanza kutekelezwa katika Mkoa wa Singida mwezi Novemba, 2020 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2021.

Mheshimiwa Spika, vijiji 16 vilivyobakia vinaendelea kupatiwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa REA wa kusambaza umeme vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ulioanza kutekelezwa mwezi Machi, 2021 na utakaokamilika mwezi Desemba, 2022. Gharama ya mradi ni bilioni 8.47.
MHE. NOAH L.S. MOLLEL aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itawalipa fidia ya kupisha njia kubwa ya umeme wananchi wa Vijiji vya Lengijape, Ilkurot na Olkejulenderit katika Jimbo la Arumeru Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Noah Lemburis Saputu Mollel, Mbunge wa Arumeru Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Umeme TANESCO inaendelea kukamilisha ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Singida hadi Namanga. Lengo kuu la mradi huu ni kuimarisha upatikanaji wa umeme katika Gridi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO imeshalipa fidia kwa wananchi wote jumla ya shilingi bilioni 52.67 zikiwa ni fidia kwa wananchi 4,526 katika mikoa yote mitatu iliyoguswa na mradi huu wakiwemo wananchi wa Vijiji vya Lengijape, llkurot na Olkejulenderit katika Jimbo la Arumeru Magharibi. Aidha, Serikali kupitia TANESCO imeshalipa fidia kwa taasisi zilizopo katika vijiji vyote vya Wilaya za Singida Vijijini, Hanang, Babati na Longido.

Mheshimiwa Spika, maandalizi ya ulipaji wa fidia shilingi bilioni 314.675 kwa maeneo ya taasisi na vijiji 38 katika Wilaya za Monduli, Arumeru na Manispaa ya Sindida yanaendelea na maeneo ya vijiji na taasisi hizo yatalipwa fidia kupitia Wakurugenzi wa Halmashauri husika ifikapo mwezi Juni, 2021.
MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itakamilisha kazi ya kupeleka umeme vijiji 49 vya Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe ambavyo bado haijapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Timotheo Paul Mnzava, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 49 vilivyobaki katika Wilaya ya Korogwe ilianza mwezi Mei, 2021 na kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivi itakamilika ifikapo mwezi Septemba, 2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, kazi ya utekelezaji wa mradi huu inahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 urefu wa kilometa 289.4, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 urefu kilometa 45, ufungaji wa transfoma 50 zenye uwezo wa KVA 50 pamoja na kuunganisha huduma ya umeme wateja wa awali 990. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 12.85.
MHE. SILVESTRY F. KOKA aliuliza:-

Mradi wa kusambaza umeme katika Jimbo la Kibaha Mjini unakwenda kwa kusuasua:-

Je, ni lini Mradi huo utakamilika ili Wananchi wa Kibaha Mjini waondokane na adha ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kusambaza umeme kwa Wilaya ya Kibaha Mjini (Peri-Urban) ulianza mwezi Novemba, 2019. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2021.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yanayonufaika na mradi huu ni pamoja na Pangani, Maili Moja, Picha ya Ndege na Sofu. Gharama ya Mradi ni shilingi bilioni 18.56.
MHE. SEBASTIAN S. KAPUFI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kasi ya kufikisha umeme wa msongo mkubwa katika Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sebastian Simon Kapufi, Mbunge wa Mpanda Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa gridi ya Taifa kwa msongo wa kilovolti 132 yenye urefu wa kilometa 381 kutoka Tabora hadi Katavi na ujenzi wa vituo vitatu vya kupoza umeme vya msongo wa kilovolti 132 kwenda 133 vya Ipole, Inyonga na Mpanda. Ujenzi wa majengo ya vituo vya kupooza umeme vya Ipole na Inyonga pamoja na uzio umekamilika kwa takribani asilimia 90. Mradi unatarajia kukamilika ifikapo Agosti, 2023, gharama ya mradi ni Shilingi Bilioni 64.9.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia inaendelea na utaratibu wa ujenzi wa njia kuu ya kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 kutoka Iringa, Mbeya, Tunduma, Sumbawanga kupitia Mpanda hadi Kigoma takribani kilometa 1,232. Kazi inayofanyika kwa sasa ni kukamilisha taratibu za kupata Mtaalamu Mshauri wa kuandaa nyaraka za kumpata Mkandarasi wa kuanza ujenzi wa mradi. Ujenzi wa mradi unatarajiwa kuanza Novemba, 2022 na kukamilika mwezi Oktoba, 2024. Gharama ya mradi ni Shilingi Bilioni 470.42.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Jimbo la Tunduru Kusini lina Vijiji sita kati ya 65 vyenye umeme.

(a) Je, ni lini REA Awamu ya Tatu utaanza?

(b) Je, ni lini umeme wa ujazilizi wa maeneo ambayo bado umeme haujafika hasa Vitongoji vya Vijiji vya Azimio, Chiwana, Umoja, Mkandu, Mbesa, Airport, Namasalau, Tuwemacho, Ligoma, Mchuruka na Makoteni vitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini lenye sehemu (a) na
(b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa mradi wa kupeleka umeme wa REA Awamu ya Tatu mzunguko wa Pili ulianza mwezi Machi, 2021. Mradi huu utakamilika ifikapo mwezi Desemba, 2022. Katika jimbo la Tunduru Kusini Vijiji vyote vilivyobaki vitapelekewa umeme kupitia mradi huu wa REA-III unaoendelea kupitia Kampuni Mbili za Wakandarasi M/S JV Guangdong Jianneng Electric Power Engineering CO. LTD na White City International Contractors LTD. Gharama ya Mradi ni shilingi bilioni 27.25.

Mheshimiwa Mwenyekiti, usambazaji wa umeme wa ujazilizi katika vijiji vya Jimbo la Tunduru Kusini vikiwemo vitongoji vya Vijiji vya Azimio, Chimwana, Umoja Mkandu, Mbesa, Airport, Namesalau, Tuwemacho, Ligoma, Mchuruka na Makoteni utaanza mwezi Septemba, 2021 na kukamilika mwezi Desemba, 2022.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza: -

(a) Je, ni Vijiji vingapi vya Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya vimepata umeme wa REA II, Densification na REA III?

(b) Je, ni lini vijiji vilivyobaki vitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mbeya Vijijini ina jumla ya vijiji 140. vijiji 101 vina umeme ambao umepatikana kupitia miradi mbalimbali kama ifuatavyo;

REA II Vijiji 21; ujazilizi (Densification) vijiji 24; na mradi wa REA awamu ya tatu mzunguko wa kwanza vijiji 45. Vijiji 11 vimepatiwa umeme kupitia miradi inayotekelezwa na Shirika la Umeme nchini (TANESCO).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 39 vilivyobaki ilianza mwezi Mei, 2021 na kazi hiyo, itakamilika ifikapo Disemba, 2022. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 8.05.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza:-

Je, ni lini wananchi wa Makambako watalipwa fidia baada ya maeneo yao kuchukuliwa na Serikali kwa ajili yakuzalisha umeme wa upepo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika juhudi za kuongeza upatikanaji wa umeme nchini kupitia vyanzo mbalimbali, eneo la Kijiji cha Majengo Jijini Makambako, limebainika kuwa na uwezo wa kuwekewa miundombinu ya kuzalisha umeme kupitia nishati ya upepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inakamilisha taratibu za kuingia Mkataba wa uzalishaji wa umeme wa upepo na Mwekezaji Binafsi aitwaye Sin Tan. Kwa mujibu wa Mkataba huo, fidia kwa wananchi wa maeneo yatakayotumika kuzalisha umeme huo, italipwa na mwekezaji huyo, katika kipindi cha kuanzia mwezi Agosti, 2021 na Julai, 2022 ambacho ni kipindi kinachotarajiwa kutekelezwa kwa mradi huo.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itamaliza ujenzi wa umeme wa Grid ya Taifa Mkoani Katavi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inaendelea na utekelezaji wa Mradi wa Ujenzi wa Njia Kuu ya Kusafirisha Umeme wa Gridi ya Taifa wa msongo wa kilovolti 132, yenye urefu wa kilometa 381 kutoka Tabora hadi Katavi. Mradi huu unahusisha pia ujenzi wa vituo vitatu vya kupoza umeme vya msongo wa kilovoti 132 kwenda 33 vya Ipole, Inyonga na Mpanda. Ujenzi wa Mradi unatarajia kukamilika ifikapo mwezi Agosti, 2023. Gharama ya mradi ni Shilingi Bilioni 64.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ujenzi wa mradi mwingine wa njia ya kusafirisha umeme mkubwa wa kilovoti 400 kutoka Iringa - Mbeya – Sumbawanga – Mpanda hadi Kigoma yenye urefu wa kilometa 1,232, unatarajiwa kuanza Novemba na kukamilika mwezi Oktoba, 2024. Gharama ya mradi ni Shilingi Bilioni 470.42.
MHE. AYSHAROSE N. MATTEMBE aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme katika vijiji 14 vya Jimbo la Manyoni Magharibi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aysharose Ndogholi Mattembe, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kazi ya kupeleka umeme katika vijiji 14 pamoja na vijiji vingine vilivyobaki katika Jimbo la Manyoni Magharibi itaanza mwezi Julai, 2021 kupitia utekelezaji wa mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili. Mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Disemba, 2022.

Mheshimiwa Spika, kazi ya utekelezaji wa mradi huu katika Wilaya ya Manyoni kwa ujumla inahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 urefu wa kilometa 383.1, njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4 urefu kilometa 31, ufungaji wa transfoma 31 zenye uwezo wa KVA 50 pamoja na kuunganisha huduma ya umeme kwa wateja wa awali 682. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 15.45.
MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza: -

Je, ni lini Vijiji na Kata katika Jimbo la Singida Kaskazini ambavyo havijapata umeme vitapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhani, Mbunge wa Singida Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, vijiji 26 vya Jimbo la Singida Kaskazini ambavyo havijapata umeme kati ya vijiji 84 vitapelekewa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ulioanza mwezi Machi, 2021. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2021 na gharama ya mradi ni shilingi bilioni 26.6.
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y. MHE. SHAMSIA A. MTAMBA aliuliza: -

Serikali ilikuwa na mpango mzuri juu ya uwepo wa nishati ya gesi asilia nchini, lakini mpaka sasa kumekuwa na sintofahamu juu ya mwendelezo wa uwekezaji wa miradi hiyo ikiwemo gesi ya Mkoa wa Mtwara.

Je, nini kauli ya Serikali juu ya mwendelezo wa miradi hii nchini?
NAIBU WAZIRI NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shamsia Azizi Mtamba Mbunge wa Mtwara Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo ya Petroli nchini (TPDC) inaendelea na uwekezaji katika sekta ya rasilimali ya gesi nchini kuanzia shughuli za utafutaji, uchorongaji na uendelezaji wa shughuli hizo.

Mheshimiwa Spika, hadi sasa takribani mikataba 11 ya utafutaji na uchimbaji wa gesi asilia inaendelea kufanyiwa kazi kati ya makampuni mbalimbali ya uwekezaji kwa ushirikiano na Serikali kupitia TPDC. Hadi sasa gesi iliyogunduliwa imefikia futi za ujazo trilioni 57.54. Sehemu ya gesi hii hutumika katika kuzalisha umeme kwa asilimia zaidi ya 50 ya umeme wote nchini, lakini pia viwandani, katika majumba na katika magari.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha kuwa gesi hiyo inaendelea kunufaisha Taifa, Serikali inaendelea kutekeleza mradi mkubwa wa kimkakati wa kuchakata gesi kuwa katika kimiminika (Liquefied Natural Gas – LNG) unaotarajiwa kuanza ujenzi ifikapo mwaka 2023. Serikali kupitia tayari imelipa fidia ya shilingi bilioni 5.71. Gharama ya mradi ni dola za Marekani bilioni 30.5. Mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo Juni, 2028.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itawasha umeme kwenye Vijiji na Vitongoji vyote katika Jimbo la Arumeru Mashariki ambavyo umeme bado haujawashwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote ambavyo havijapata umeme katika katika Jimbo la Arumeru Mashariki vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA awamu ya tatu, mzunguko wa pili ulioanza Mwezi Machi, 2021. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika Mwezi Disemba, 2022. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 2.07.

Mheshimiwa Naibu Spika, vitongoji vya Jimbo la Arumeru Mashariki ambavyo havijafikiwa na umeme vitaendelea kupatiwa umeme kupitia mradi wa ujazilizi yaani densification unaotarajiwa kuanza mwezi Julai, 2021. Aidha, kazi ya kupeleka umeme katika vitongoji ni endelevu, Serikali kupitia TANESCO na REA itaendelea kupeleka umeme katika vitongoji kulingana na upatikanaji wa fedha.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Mradi wa Ujazilizi katika Mkoa wa Manyara na Jimbo la Mbulu Vijijini ili kuwafikia wananchi wengi ambao hawakupitiwa na Mradi wa REA I, II na III?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inaendelea na utekelezaji wa miradi ya ujazilizi kupitia mpango wa kupeleka umeme vijijini, ili kufikisha umeme katika vitongoji vya Tanzania Bara vikiwemo vitongoji vya Jimbo la Mbulu Vijijini. Miradi hii inatekelezwa awamu kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha Mwaka 2021/2022, jumla ya vitongoji 246 katika Mkoa wa Manyara vikiwemo vitongoji vyote visivyo na umeme katika Jimbo la Mbulu Vijijini vinatarajiwa kufikishiwa umeme. Gharama ya Mradi ni shilingi bilioni 45. Zoezi la kupeleka umeme katika vitongoji ni endelevu linalotekelezwa kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) pamoja na TANESCO.
MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza: -

Je, ni lini Mkandarasi wa umeme wa REA ataanza kazi ya kusambaza umeme katika Jimbo la Tunduru Kusini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imeanza kusambaza umeme nchini kuanzia Mwezi Mei, 2021 ambapo Kampuni ya M/S Guangdong Jianneng Electric Power Engineering Co. LTD imepewa kazi hiyo katika Wilaya ya Tunduru ikiwa ni pamoja na Jimbo la Tunduru Kusini.

Mheshimiwa Spika, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilomita 639 za njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33, njia za umeme msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilomita 80, ufungaji wa transfoma 80 na uunganishaji wa wateja wa awali wapatao 1,760. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 36.67.

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi kwa sasa anakamilisha usanifu wa kina na uletaji wa vifaa vya ujenzi wa miundombinu ya umeme. Mradi unatarajiwa kukamilika Mwezi Desemba, 2022 na kufikisha huduma ya umeme katika vijiji vyote 80 vilivyokuwa vimebaki bila umeme katika Wilaya ya Tunduru.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza: -

(a) Je, kwa nini TANESCO imewaondoa watumiaji wadogo wa umeme chini ya unit 75 katika Vijiji vya Itigi, Majengo, Ziginali, Tambukareli, Songambele na Mlowa kuwa Mitaa badala ya Vijiji?

(b) Je, ni lini wanavijiji hao watarudishwa katika matumizi ya watumiaji wadogo kwa kuwa hivi ni Vijiji na si Mitaa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Agizo la kurekebisha bei la EWURA Na. 2016-010 la Mwaka 2016, kupitia masharti Namba (h) na (i) inaelekeza TANESCO, kuwaunganisha wateja wapya wa majumbani walio maeneo ya vijijini katika kundi la D1 yaani Domestic 1. Kupitia mfumo wa njia moja ya umeme na wateja walio katika kundi la D1 watahamishiwa kwenda T1 ambayo ni Tariff 1. Endapo manunuzi yao katika kipindi cha miezi mitatu mfululizo yatazidi wastani wa unit 75 kwa mwezi.

Mheshimiwa Spika, wateja wa Itigi walihamishiwa kwenda kundi la T1 kwa kuwa wapo Itigi mjini. Kwa sasa, TANESCO inaendelea kuchambua hali ya ununuzi wa umeme kwa wateja hawa. Kwa lengo la kubaini waliokidhi vigezo vya kuwa kwenye kundi la D1 kwa mujibu wa Agizo la EWURA. Zoezi hili linatarajia kukamilika ifikapo tarehe 30 Novemba, 2021. Baada ya zoezi hili kukamilika wanaostahili kuwa kwenye kundi la Tariff D1 watapelekwa kwenye kundi hili Disemba, 2021.
MHE. TASKA R. MBOGO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Umeme wa Grid ya Taifa katika Mkoa wa Katavi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Taska Restituta Mbogo Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na utekelezaji wa Mradi wa ujenzi wa njia kuu ya kusafirisha umeme wa Gridi ya Taifa wa msongo wa kilovolti 132 yenye urefu wa kilometa 381 kutoka Tabora hadi Katavi na ujenzi wa vituo vitatu (3) vya kupoza umeme vya msongo wa kilovolti 132/ 33kV Ipole (Sikonge), Inyonga (Mlele) na Mpanda (Mpanda Mjini).

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa majengo ya kudhibiti mfumo wa umeme (Control Building) ya Ipole, Inyonga na Mpanda yamekamilika. Upimaji wa mkuza (wayleave) kwa ajili ya ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme (Transmission Line) kutoka Tabora hadi Katavi umekamilika. Zoezi la uthamini wa mali za wananchi katika maeneo yanayopitiwa na mradi limekamilika kwa Wilaya za Mlele na Mpanda Mjini na zoezi hilo linaendelea kwa Wilaya za Tabora, Uyui, na Sikonge na litakamilika mwishoni mwa mwezi wa Novemba, 2021. Mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo Agosti, 2023.

Mheshimiwa Spika, gharama ya mradi ni shilingi bilioni 64.9 na fedha hizi zote ni fedha za ndani na ujenzi unafanywa na Wataalamu wa Shirika la TANESCO.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA aliuliza: -

(a) Je, nini matokeo ya Utafiti wa mafuta uliofanyika katika Ziwa Tanganyika zaidi ya miaka mitatu iliyopita?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuvuna mafuta hayo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kilumbe Shabani Ng’enda, Mbunge wa Kigoma Mjini, lenye sehemu
(a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, utafiti wa mafuta katika Ziwa Tanganyika umegawanywa katika vitalu viwili; Kaskazini na Kusini. Katika kipindi cha mwaka 2015/2016, TPDC ilikusanya taarifa za uvutano wa usumaku zenye jumla ya urefu wa kilomita 24,027 za mstari katika kitalu cha Ziwa Tanganyika Kaskazini. Tathmini ya taarifa hizo pamoja na taarifa za kijiolojia na kijiofizikia zilizopatikana katika eneo la mradi zimewezesha kugundua na kutenga maeneo yenye uwezekano wa kuwepo kwa mashapo ya kuhifadhi rasilimali (petroleum).

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Shirika la Maendeleo Nchini (TPDC) kwa kushirikiana na Mwekezaji kutoka Kampuni ya Beach Petroleum ilifanya utafiti wa mafuta katika kitalu cha Ziwa Tanganyika Kusini kuanzia mwaka 2010 mpaka mwaka 2017. Taarifa za utafiti huo ziliwezesha kubaini miamba yenye uwezekano wa kuhifadhi mafuta. Hata hivyo, changamoto za uchimbaji kisima katika Ziwa Tanganyika zilizomkabili Mwekezaji alishindwa kusafirisha vifaa vya kuchoronga kutokana na kina kirefu cha maji katika Ziwa Tanganyika na upatikanaji wa fedha zilisababisha Mwekezaji kushindwa kuendelea na utafiti na hivyo kulazimika kurudisha kitalu kwa Serikali mnamo mwaka 2017 kwa kuzingatia sheria zetu za mafuta na gesi.

Mheshimiwa Spika, pamoja na uwepo wa viashiria vizuri vya mafuta katika vitalu vya Ziwa Tanganyika, mpaka sasa Serikali haijagundua mafuta wala gesi katika eneo hilo. Katika mwaka wa fedha 2021/2022 TPDC inatarajia kuendelea kufanya tathmini ya kina ya takwimu za usumaku kwa Kitalu cha Ziwa Tanganyika Kaskazini. Takwimu hizi zitatumika kutengeneza mpango wa kukusanya takwimu za mitetemo kwa ajili ya kuainisha na kuhakiki uwepo wa mashapo ya kuhifadhi mafuta na gesi. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafikisha umeme katika Kata za Nyanzwa, Udekwa na Ukwega Wilayani Kilolo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lazaro Justin Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kilolo ina kata 21, kati yake kata tatu tu hazijapata umeme na vijiji 94, kati yake vijiji 23 tu havijapata umeme. Vijiji vyote 23 ambavyo havina umeme vikiwemo Vijiji vya Kata za Nyanzwa, Udekwa na Ukwega ambavyo ni Nyanzwa, Mgowelo, Igunda, Udekwa, Wotalisoli, Ifuwa, Ukwega, Ipalamwa, Makungu na Mkalanga vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ambao utekelezaji wake ulianza mwezi Machi, 2021 na unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.
MHE. LUHAGA J. MPINA Aliuliza: -

(a) Je, ni sababu gani zilizopelekea kuchelewa kukamilika kwa ujenzi wa Bwawa la kufua umeme wa maji la Julius Nyerere?

(b) Je, kwa nini Mkandarasi ameshindwa kujaza maji kwenye Bwawa kufikia tarehe 15 Novemba, 2021 kama ilivyokuwa imekubalika?

(c) Je, ni hatua gani zimechukuliwa kutokana na ucheleweshwaji huo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama walivyosema wenzangu, nami kabla ya kujibu swali nimshukuru sana Mwenyekiti Mungu kwa afya na amani, lakini pia nimshukuru Rais, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuniamini kuhudumu katika nafasi hii ya Naibu Waziri wa Nishati. Pia niwapongeze Waheshimiwa Wabunge wenzangu wote kwa uchaguzi mkubwa, wa maajabu na wa furaha tulioufanya jana hapa Bungeni wa kumchagua Mheshimiwa Spika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Luhaga Joelson Mpina, Mbunge wa Kisesa lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wa kukamilika kwa mradi kimkataba ni tarehe 14 Juni, 2022. Tarehe hiyo bado haijafikiwa.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, ili bwawa la Mwalimu Julius Nyerere lianze kujazwa maji, ni sharti liwe limejengwa kufikia kimo cha mita 95 juu ya usawa wa bahari ambapo kazi hiyo imekamilika. Aidha, ilitakiwa handaki lililojengwa kuchepusha maji ya Mto Rufiji kuzibwa. Kazi ya kuziba au kufunika handaki kwa kutumia vyuma maalum vizito ilihitaji mfumo maalum ambao ni wa kudumu wa mitambo ya kubebea milango hiyo (Hoist Crane system) kuwepo katika eneo la mradi. Mfumo huo unatengenezwa mahsusi kwa ajili ya kazi hii na kazi hii inapoisha crane hizo huondolewa na hazitumiki kwa kazi nyingine. Mitambo hiyo ilichelewa kufika kwa wakati kutokana na viwanda kufungwa na safari za meli kuathiriwa kutokana na UVIKO 19. Milango na mtambo wa kubebea tayari imefika na kazi za kuifunga zinatarajiwa kukamilika mwezi Machi, 2022.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Wizara ya Nishati na TANESCO inaendelea kumsimamia mkandarasi aongeze kasi ya utekelezaji wa ujenzi ili kufidia muda uliopotea kwa kuongeza wafanyakazi na muda wa kazi.
MHE. DKT. JOHN D. PALLANGYO Aliuliza: -

Je, lini Serikali itawaunganishia umeme wa REA wananchi wa Vijiji vilivyopo katika Kata za Jimbo la Arumeru Mashariki ambazo hazina umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI Alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa John Danielson Pallangyo, Mbunge wa Arumeru Mashariki kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Arumeru Mashariki lina jumla ya Kata 26 na vijiji 90. Ni vijiji 12 tu ambavyo havina umeme na sasa vinapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaotekelezwa katika Jimbo la Arumeru Mashariki. Kazi zinazofanyika sasa ni usanifu wa kina, upimaji, uandaaji wa michoro na manunuzi ya vifaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi huu unahusisha ujenzi wa njia za umeme ya msongo kilovoti 33 zenye urefu wa kilomita 40.30; kilomita 12 ya njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4; ufungwaji transfoma 12 za KVA 50; pamoja na kuunganisha wateja wa awali 264. Gharama ya mradi ni shilingi bilioni 2.071 na utekelezaji wake unatarajiwa kukamilika Mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine Serikali imefanya uhakiki na kuainisha uwepo wa vitongoji takriban 37,610 visivyokuwa na umeme Tanzania Bara na inakadiriwa kuwa shilingi trillion 7 zitahitajika ili kukamilisha mahitaji ya umeme katika vitongoji hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekwishaanza utekelezaji wa miradi ya ujazilizi unaolenga kufikisha umeme katika vitongoji vyote Tanzania Bara awamu kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha ikiwa ni pamoja na Vitongoji vya Jimbo la Arumeru Mashariki.
MHE. FLATEI G. MASSAY Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza ahadi yake ya kupeleka umeme katika Vijiji na Vitongoji vya Jimbo la Mbulu Vijijini?
NAIBU WAZIRI WAZIRI WA NISHATI Alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Mbulu vijijini lina jumla ya vijiji 76 na vitongoji 362. Ni vijiji 42 tu ambavyo havina umeme katika Jimbo la Mbulu Vijijini na sasa vinapatiwa umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaotekelezwa katika Jimbo hilo. Kazi zinazofanyika sasa ni manunuzi ya vifaa na ujenzi wa miundombinu ya umeme. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mnamo mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika hatua nyingine Serikali imefanya uhakiki na kuainisha uwepo wa vitongoji takriban 37,610 visivyokuwa na umeme Tanzania Bara na inakadiriwa kuwa shilingi trillion 7 zitahitajika ili kukamilisha mahitaji ya umeme katika vitongoji hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekwishaanza utekelezaji wa miradi ya ujazilizi unaolenga kufikisha umeme katika vitongoji vyote Tanzania Bara awamu kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha ikiwa ni pamoja na Vitongoji vya Jimbo la Mbulu Vijijini.
MHE. FESTO R. SANGA aliuza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kutekeleza Mradi wa REA katika Wilaya ya Makete ili kuhakikisha umeme unafika kila Kijiji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Makete ina jumla ya vijiji 93 na vijiji 56 vimekwisha fikishiwa umeme. Vijiji 37 ambavyo havikuwa na umeme vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA awamu ya III, mzunguko wa pili unaoendelea kutekelezwa na Mkandarasi M/S JV Silo Power Limited na Guangzhou Yidian Equipment Installation Company Limited. Mkandarasi anaendelea na kazi ya usanifu wa kina, upimaji, uandaaji wa michoro na manunuzi ya vifaa.

Mheshimiwa Spika, Mradi wa kupeleka umeme katika Wilaya ya Makete unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kilovoti 33, zenye urefu wa kilomita 222.5; kilomita 37 ya njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4; ufungwaji transfoma 37 za KVA 50; pamoja na kuunganisha wateja wa awali 814. Gharama ya mradi ni Shilingi bilioni 9.95 na utekelezaji unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2022.
MHE. COSATO D. CHUMI K.n.y. MHE. FRANCIS L. MTEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha kuvipatia umeme wa REA Vitongoji na Vijiji vilivyobaki katika Jimbo la Mbarali?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Leonard Mtega, Mbunge wa Mbarali, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mbarali ina jumla ya vijiji 102. Ni vijiji 20 tu ambavyo bado havijapatiwa umeme. Vijiji hivyo 20 vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa REA mzunguko wa Pili awamu ya Tatu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi huu unaendelea kutekelezwa na Mkandarasi ambaye ni M/S Electrical Transmission and Distribution Construction and Maintenance Co. LTD. Mkandarasi amekamilisha kazi ya usanifu wa kina, upimaji, uandaaji wa michoro na anaendelea na manunuzi ya vifaa pamoja na kusimika nguzo katika maeneo ya mradi. Gharama ya mradi ni Shilingi bilioni saba na utekelezaji unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa vitongoji, Serikali imeshaanza utekelezaji wa miradi ya ujazilizi unaolenga kufikisha umeme katika vitongoji vyote Tanzania Bara awamu kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha ikiwa ni pamoja na Vitongoji vya Jimbo la Mbarali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine, Serikali imefanya uhakiki na kuainisha uwepo wa vitongoji takribani 37,610 visivyokuwa na umeme Tanzania Bara na inakadiriwa takribani shilingi trilioni saba zitahitajika ili kukamilisha mahitaji ya umeme katika vitongoji hivyo vyote.
MHE. GRACE V. TENDEGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka Umeme wa REA kama ilivyoahidi katika Vijiji vya Kitayawa, Kipera, Lupalama, Itagutwa, Ikungwe na Lyamgungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Grace Victor Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Vijiji vya Kipera, Itagutwa, Ikungwe, Lupalama na Lyamgungwe vimepata umeme kupitia mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Kwanza. Kazi iliyobaki ni kufikisha umeme katika vitongoji vya vijiji hivyo vilivyobaki bila umeme katika miradi ya ujazilizi (densification) kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO imeshapeleka umeme katika Kitongoji cha Kitayawa ambacho kipo katika Kijiji cha Tagamenda Kata ya Luhota, Wilaya ya Iringa. Aidha, TANESCO pamoja na REA wanaendelea kuunganisha umeme kwa wateja wa Kitongoji cha Kitayawa na vitongoji vingine vya Jimbo la Iringa Mjini na Iringa kwa ujumla kadri ya upatikanaji wa fedha. (Makofi)
MHE. MASACHE N. KASAKA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itafikisha umeme kwenye vijiji ambavyo bado havijafikiwa Wilayani Chunya pamoja na Makao Makuu ya Kata za Nkung’ungu, Lualaje, Mafyeko na Kambikatoto?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Masache Njelu Kasaka, Mbunge wa Lupa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu – Mzunguko wa Pili unaolenga kufikisha miundombinu ya umeme katika vijiji vyote ambavyo vilikuwa havijafikiwa na huduma ya umeme Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, Wakala wa Nishati Vijijini (REA) kwa niaba ya Serikali umeingia mkataba na Kampuni ya M/S Electrical Transmission and Distribution Construction and Maintenance Company Limited kutekeleza mradi huu katika Mkoa wa Mbeya ambao utekelezaji wake umekwishaanza kwa Mkandarasi kukamilisha uhakiki na kuagiza vifaa vitakavyotumika katika ujenzi.

Mheshimiwa Spika, mradi wa kupeleka umeme katika Wilaya ya Chunya unahusisha ujenzi wa njia ya umeme ya msongo kilovoti 33 zenye urefu wa kilomita 245.5; kilomita 12 ya njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 0.4; ufungwaji transfoma 12 za KVA 50; pamoja na kuunganisha wateja wa awali 814. Gharama ya mradi ni Shilingi bilioni 10.656 na utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.
MHE. REHEMA J. MIGILLA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itatekeleza mchakato wa Wilaya ya Urambo na Kaliua kutumia line yake ya umeme ili kupunguza au kumaliza tatizo la kukatika kwa umeme katika Wilaya hizo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rehema Juma Migilla, Mbunge wa Ulyankulu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya za Urambo na Kaliua zinapata umeme kwa njia moja inayoanzia Kituo cha Kupooza Umeme kilichopo Tabora Mjini. Serikali kupitia Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) inatekeleza mradi wa ujenzi wa Kituo cha Kupooza Umeme katika Kijiji cha Uhuru, Wilayani Urambo, kitakachopokea umeme mkubwa (Kilovolt 132) kutoka Tabora Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, utekelezaji wa mradi unaendelea, jengo la kupokelea Umeme (Control Building) limekamilika, upimaji wa njia ya msongo wa kilovoti 132 kutoka Tabora hadi Urambo umekamilika, uthamini wa mali za wananchi watakaopitiwa na mradi umekamilika na mikataba ya wazabuni watakaoleta vifaa vitakavyotumika kwenye ujenzi (wa njia na vifaa vya umeme) imekamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kituo hicho kitakuwa na njia za usambazaji umeme (distribution lines) zinazojitegemea kwa kila Wilaya, yaani Urambo moja na Kaliua moja na hivyo kufanya ziwe na Umeme wa Uhakika zaidi. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba, 2022.
MHE. NEEMA W. MGAYA K.ny. MHE. FESTO R. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mto Lumakali Wilayani Makete?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea na maandalizi ya utekelezaji wa Mradi wa Rumakali wa kuzalisha megawati 222 ulioko katika Wilaya ya Makete, Mkoani Njombe.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2022/2023 Serikali imetenga shilingi bilioni nane kwa ajili ya maandalizi ya awali ya mradi wa Rumakali. TANESCO imehuisha upembuzi yakinifu pamoja na kukamilisha nyaraka za zabuni za kumpata mkandarasi wa ujenzi. Aidha, uthamini wa mali za wananchi zinazopitiwa na mradi utakamilika mwezi Oktoba, 2022. Utekelezaji wa mradi huu unatarajiwa kuanza mwaka ujao.
MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE K.n.y. MHE. REUBEN N. KWAGILWA
aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka umeme mitaa 28 ya Jimbo la Handeni Mjini ambayo bado haijapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Reuben Nhamanilo Kwagilwa, Mbunge wa Handeni Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Jimbo la Handeni Mjini lina jumla ya mitaa 60. Kati ya mitaa hiyo 32 ina umeme sawa na asilimia 53.3 na mitaa 28 haina umeme sawa asilimia 46.7.

Mheshimiwa Spika, Mitaa yote 28 ya Handeni Mjini ipo katika mpango wa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa Umeme Vijijini, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, unaotekelezwa na mkandarasi kampuni ya Derm Electrics Tanzania ambaye yupo eneo la kazi na anaendelea na ujenzi wa miundombinu ya umeme katika maeneo mbalimbali ya Wilaya ya Handeni.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa mradi huu utakamilika Mwezi Desemba, 2022.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaweka Kituo cha kupoza umeme Igunga?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicholaus George Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO imebaini uhitaji wa vituo vya kupoza umeme katika Wilaya zote Tanzania Bara zenye uhitaji huo. Aidha, imeweka mpango wa ujenzi wa vituo hivyo kulingana na uhitaji kuanzia mwaka huu wa fedha 2022/2023. Kituo cha Kupoza umeme cha Igunga kitawekwa katika mpango wa ujenzi wa mwaka ujao.

Mheshimiwa Spika, ili kuimarisha huduma ya umeme katika maeneo ya Wilaya ya Igunga na Nzega, Serikali inaendelea na mradi wa upanuzi wa kituo cha kupoza umeme cha Lusu kilichopo Wilayani Nzega kutoka MVA 15 132/33kV hadi MVA 60 132/33kV. Upanuzi huu, utakamilika ndani ya mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. ABEID R. IGHONDO aliuliza: -

Je, ni lini mradi wa kufua umeme wa upepo na jua wa MW 100 utaanza rasmi katika Halmashauri ya Wilaya ya Singida?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abeid Ighondo Ramadhan, Mbunge wa Singida Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mwekezaji aitwaye Upepo Energy alifanikiwa kushinda zabuni ya kuendeleza miradi miwili ambapo Megawatt 100 za umeme zitazalishwa kwa nguvu ya upepo na Megawatt 45.08 zitazalishwa kwa nguvu ya jua.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa majadiliano baina ya TANESCO na Mwekezaji kuhusu bei ya kuuziana umeme (PPA) yamekamilika. Majadiliano kuhusu mkataba wa utekelezaji (Implementation Agreement-IA) yanaendelea. Ipo changamoto ya mwekezaji kuhitaji “Government Guarantee” kinyume na Sera ya Serikali na masharti ya zabuni kama ilivyotangazwa. Iwapo mwekezaji atakubali kutekeleza mradi huu bila masharti mapya aliyoweka, mradi huu utaanza kutekelezwa mwezi Januari, 2023.
MHE. INNOCENT S. BILAKWATE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vitongoji ambavyo havijafikiwa na huduma ya umeme katika Kata za Businde, Bugara na Kibale?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Innocent Sebba Bilakwate, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati ambaye ni Mbunge wa Kyerwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Kyerwa ina jumla ya kata 24. Kati ya Kata hizo, kata 21 tayari zina umeme na kata tatu ambazo ni Businde, Bugara na Kibale zenye vijiji 11 zitapata umeme kupitia Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili (REA III Round II). Kwa sasa, mkandarasi yupo kwenye Kata hizo anaendelea na kazi ya kusambaza umeme katika vijiji 11 kati ya vijiji 29 vilivyopo kwenye wigo wa mradi huu kwa Wilaya ya Kyerwa.

Mheshimiwa Spika, Kata hizo zina jumla ya Vitongoji 62 na tunategemea Vitongoji 33 vitafikiwa na umeme awamu hii na Vitongoji vitakavyobaki vitafikiwa umeme kupitia miradi ya ujazilizi.
MHE. BENAYA L. KAPINGA K.n.y. MHE. JONAS W. MBUNDA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itajenga Kituo Kikuu cha Kupooza katika Wilaya ya Mbinga?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jonas William Mbunda, Mbunge wa Mbinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanza kutekeleza mpango wa kuimarisha Gridi ya Taifa uliopewa jina la ‘Gridi Imara’ kwa kujenga miundombinu ya usafirishaji na usambazaji umeme pamoja na vituo vya kupooza na kudhibiti umeme.

Mheshimiwa Spika, mpango huu una miradi zaidi ya 40 na utatekelezwa ndani ya miaka Mitano (5) kuanzia mwaka huu wa fedha 2022/2023 ambapo Serikali imekwishatenga jumla ya Shilingi Bilioni 500 kwa ajili ya kugharamia miradi yenye vipaumbele vya kwanza.

Mheshimiwa Spika, mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolts 220 yenye urefu wa kilometa 93.5 kutoka Songea hadi Mbinga na ujenzi wa kituo cha kupooza umeme cha ukubwa wa Megawatt Mbili mara 30, kV 220 kwenda 33 utatekelezwa kuanzia mwaka wa fedha 2024/2025 na unatarajiwa kukamilika ndani ya mwaka mmoja na nusu tangu utakapoanza. (Makofi)
MHE. FRANCIS K. NDULANE aliuliza: -

Je, ni lini wananchi wa Kitongoji cha Cheketu Somanga Kusini watalipwa fidia kupisha ujenzi wa miundombinu ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Francis Kumba Ndulane, Mbunge wa Kilwa Kaskazini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inatarajia kujenga njia ya kusafirisha umeme yenye urefu wa kilomita 190 ya msongo wa kilovoti 400 kutoka Kinyerezi hadi Somanga.

Mheshimiwa Spika, Serikali tayari imelipa jumla ya Shilingi milioni 37.5 kwa wahanga 11 kati ya 13 wanaoathiriwa na mradi huu. Wahanga wawili waliobaki walitathminiwa kuwa maeneo ya Serikali ya Kijiji cha Cheketu, lakini kumekuwepo na mgogoro baina yake na wananchi. Serikali italipa malipo hayo baada ya utatuzi wa mgogoro huo.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza: -

Je, nini mkakati wa Serikali kumaliza kero ya kukatikakatika kwa umeme Mikoa ya Kusini hasa Wilaya ya Masasi na Vijiji vyake?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hali ya upatikanaji wa umeme katika Mkoa wa Mtwara imeendelea kuimarika na kuwa ya kuridhisha ukilinganishwa na kipindi cha nyuma. Serikali inao mkakati wa dhati wa kumaliza changamoto hii kwa mikoa ya Kusini na maeneo mengine ya Tanzania nzima.

Mheshimiwa Spika, ili kuondoa changamoto hii, Serikali imetenga jumla ya shilingi milioni 600 kwa ajili ya kurekebisha miundombinu katika line za Newala, Nyangao, Masasi na Mahuta. Aidha, jumla ya shilingi bilioni 2.2 zimetengwa kwa ajili ya kujenga njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka Nanganga hadi Masasi. Pia, jumla ya shilingi bilioni mbili zimetengwa kuweka transfoma kubwa kati ya Tunduru na Namtumbo ili kupata umeme mkubwa kutoka Ruvuma bila kuathiri watumiaji wengine.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wa kudumu wa kuimarisha Gridi ya Taifa, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 250 kujenga Gridi ya Taifa kutoka Songea – Tunduru – hadi Masasi. Kwa mwaka 2022/2023 Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 66.7 kuanza ujenzi wa njia hiyo.
MHE. STANSLAUS S. MABULA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaainisha bei rasmi za kuunganisha umeme maeneo ya kata za mjini zenye sura za vijiji?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stanslaus Shing’oma Mabula, Mbunge wa Nyamagana, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na zoezi la utambuzi wa maeneo na wananchi wanaoishi katika maeneo ya Kata za Mjini zenye sura za vijiji.

Mheshimiwa Spika, zoezi hili linatarajiwa kukamilika mnamo mwezi Desemba, 2022 na baada ya zoezi hili Serikali itapanga bei muafaka za kuunganisha umeme kulingana na uhalisia wa maeneo husika.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. MOSHI S. KAKOSO aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka vifaa kingaradi katika eneo la Mwese lenye milipuko ya radi mara kwa mara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Moshi Selemani Kakoso, Mbunge wa Mpanda Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua kuwa kuna maeneo yenye matukio mengi na makubwa ya radi hususan eneo la Mwese Mkoani Katavi. Hali hii husababisha nguzo nyingi za umeme, transfoma na vifaa vingine vya umeme kuharibiwa na radi.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2022 Serikali imetenga shilingi milioni 502 kwa ajili ya ukarabati wa miundombinu ya umeme katika Mkoa wa Katavi ikiwa ni pamoja na ununuzi wa nguzo za zege, transfoma zenye kuhimili madhara ya radi (surge arresters) na kuweka waya (overhead shield wire) katika maeneo yenye matukio ya milipuko ya radi mara kwa mara ikiwemo kingaradi eneo la Mwese, ahsante.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA K.n.y. MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka ruzuku kwenye majiko madogo ya gesi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea kuweka mikakati ya kuhakikisha nchi inafikia zaidi ya asilimia 80 ya matumizi ya nishati safi ya kupikia ifikapo mwaka 2032. Miongoni mwa mikakati hiyo ni pamoja na kufanyika kwa mjadala wa Kitaifa wa nishati safi ya kupikia, kuunda kikundi kazi kwa ajili ya uratibu, kutenga fedha katika bajeti ya 2023/2024 kwa ajili ya shughuli za nishati safi ya kupikia, kuanzisha mfuko wa nishati safi ya kupikia pamoja na kuzitaka taasisi zote zenye watu zaidi ya 300 kama vile shule, vyombo vya ulinzi na usalama, Magereza na kadhalika, kutumia nishati mbadala kupikia ikiwemo gesi na kuachana na matumizi ya kuni na mkaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini inatarajia kutekeleza mradi wa majaribio kwa kutoa ruzuku ya asilimia 50 ya gharama zote (jiko, gesi, mtungi pamoja na vifaa vinavyohusiana). Katika Awamu hii vifaa vipatavyo 100,000 vitasambazwa katika Mikoa 25 ya Tanzania Bara. Naomba kuwasilisha.
MHE. KWAGILWA R. NHAMANILO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa kituo kikubwa cha kupozea umeme Kwambwembwele Vibaoni?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kwagilwa Reuben Nhamanilo, Mbunge wa Handeni, kwa niaba ya Mheshimwa Waziri wa Nishati, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeanza kutekeleza mpango wa kuimarisha Gridi ya Taifa uliopewa jina ‘Gridi Imara’ kwa kujenga miundombinu ya usafirishaji na usambazaji umeme pamoja na vituo vya kupoza na kudhibiti umeme. Mpango huu una miradi zaidi ya 40 inayotekelezwa ndani ya miaka mitano kuanzia mwaka 2022/2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mwaka 2022/2023 Serikali itajenga njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 132 kutoka Mkata kwenda Kilindi kupitia eneo la Kwambwembwele Vibaoni, Handeni Mjini. Katika mwaka wa fedha 2024/2025 kituo cha kupoza umeme kitajengwa na kupokea umeme kutoka katika njia ya Mkata/Kilindi itakayojengwa mwaka huu.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza: -

Je, ni lini ujenzi wa mradi wa umeme wa upepo Singida utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO imekuwa ikifanya jitihada za kuendeleza miradi mbalimbali ya kufua umeme nchini, ikiwemo miradi ya kuzalisha umeme kwa kutumia nishati jadidifu ya upepo katika maeneo ya Mkoa wa Singida inayotekelezwa na wawekezaji binafsi wenye nia ya kuzalisha umeme na kuiuzia TANESCO.

Mheshimiwa Spika, miradi hiyo ni pamoja na mradi wa upepo MW 50 unaotekelezwa na Kampuni ya Upepo Energy eneo la Msikii Halmashauri ya Singida Vijijini, ambapo majadiliano ya mkataba wa kuuziana umeme (Power Purchase Agreement) kati yake na TANESCO yanaendelea. MW 300 unaotekelezwa na Kampuni ya GEO Wind eneo la Kititimo Halmashauri ya Singida Mjini ambapo majadiliano baina ya Mwekezaji na Mfadhili Green Climate Fund (GCF) yanaendelea. Pia MW 100 unaotekelezwa kwa ubia wa TANESCO na kampuni ya Abu-Dhabi (Masdar) eneo la Ikungi, Halmashauri ya Wilaya ya Ikungi ambapo Upembuzi Yakinifu unaendelea.

Mheshimiwa Spika, utekelezaji wa miradi hii inatarajiwa kukamilika kati ya mwaka 2023 na 2027.
MHE. HAWA S. MWAIFUNGA aliuliza: -

Je, ni nini mkakati wa Serikali kuondoa kero ya ukatikaji wa umeme nchini hasa katika maeneo ya biashara kama Kariakoo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Subira Mwaifunga, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa tatizo la ukatikaji umeme Nchini, Serikali imebuni na imeanza utekelezaji wa Mradi kabambe wa Gridi Imara unaolenga kuboresha upatikanaji wa umeme nchini kwa kufanya uboreshaji mkubwa kwenye miundombinu ya kusafirisha na kusambaza umeme. Katika mradi huo, pamoja na kazi nyingine, jumla ya kilomita zipatazo 3,930 za njia za kusafirisha umeme zitajengwa, jumla ya vituo vikubwa vya kupoza umeme 62 vitajengwa na kilomita zipatazo 2,572 za njia za usambazaji umeme zitajengwa. Katika kutekeleza mradi huu, Serikali imetenga jumla ya shilingi bilioni 500 kwa mwaka wa fedha 2022/2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutatua changamoto ya upungufu wa umeme nchini, Serikali inaendelea na jitihada za kuongeza uzalishaji umeme kupitia vyanzo mbalimbali kama vile gesi, maji, umeme jua na upepo. Miradi hiyo iko kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji. Inatarajiwa kuwa, utekelezaji wa miradi hiyo utakapokamilika, utaondoa kabisa kero ya ukatikaji wa umeme nchini. Ahsante.
MHE.ANTON A. MWANTONA aliuliza:-

Je, ni lini mradi wa REA II utamalizika kwa Vijiji 25 vilivyobakia katika Jimbo la Rungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji 25 vilivyobaki katika Jimbo la Rungwe vitapatiwa umeme kupita Mradi wa REA III mzunguko wa pili ambapo kwa sasa Mkandarasi yupo eneo la mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa mkataba, Mkandarasi wa kazi hiyo (ETDCO) atakamilisha kazi kwenye vijiji hivyo Mwezi Desemba, 2023. Ahsante sana.
MHE. NICHOLAUS G. NGASSA aliuliza: -

Je, ni lini Kata za Mtungulu, Mwamashiga, Isakamaliwa, Kining’inila na Kinungu zitapatiwa umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nicholaus George Ngassa, Mbunge wa Igunga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata za Mtungulu, Mwamashiga, Isakamaliwa, Kining’inila na Kinungu zote zipo kwenye Mradi wa REA Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaoendelea. Mkandarasi anayetekeleza mradi huo anaitwa M/S CEYLEX ameshafika kwenye maeneo hayo. Kwa Kata ya Mtunguli, katika vijiji viwili kati ya vijiji vitatu ambavyo ni Maguguni na Mtungulu, kazi ya kusambaza umeme imekamilika na umeme umeshawashwa, isipokua Kijiji cha Mwajijambo ambacho kazi ya kuvuta nyaya inaendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa Kata za Mwamashiga, Isakamaliwa, Kining’inila na Kinungu kazi ya uchimbaji mashimo na usimikaji nguzo inaendelea. Utekelezaji wa miradi hii yote unategemewa kukamilika ndani ya kipindi cha mkataba ambacho kinaishia mwezi Aprili, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. ANNA R. LUPEMBE aliuliza: -

Je, ni lini Kijiji cha Kanonge Kata ya Nsimbo kitapelekewa umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anna Richard Lupembe, Mbunge wa Nsimbo, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kijiji cha Kanoge kilichopo Kata ya Nsimbo kina jumla ya vitongoji vitano vya Kanoge A, Kanoge B, Tupindo, Kavikonge na Tulieni. Kijiji cha Kanoge tayari kimefikiwa na huduma ya umeme katika vitongoji vya Kanoge B na Tulieni. Vitongoji vitatu vilivyosalia vitafikishiwa umeme kupitia Mradi wa kusambaza umeme wa Kitongoji kwa Kitongoji (Hamlet Electrifiction Project) unaotajariwa kutekelezwa nchi nzima kulingana na upatikanaji wa fedha, ahsante.
MHE. JACKSON G. KISWAGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka transfoma yenye uwezo mkubwa wa njia tatu katika Kijiji cha Nyamihuu Kata ya Nzihi Jimboni Kalenga?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jackson Kiswaga, Mbunge wa Kalenga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Nyamihuu ni miongoni mwa vijiji vilivyopata huduma ya umeme kupitia miradi ya usambazaji wa umeme vijijini awamu ya kwanza (REA I) na kufungiwa transfoma ya KVA 100. Huduma ya umeme katika kijiji hiki imesambazwa katika vitongoji nane kati ya vitongoji 12. Vitongoji vinne vilivyobaki vimewekwa kwenye mpango wa kusambaza umeme jazilizi unaotarajiwa kutekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) katika mwaka wa fedha 2022/ 2023.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, katika bajeti ya mwaka 2022/2023, Serikali imepanga kuongeza transfoma ya pili yenye uwezo wa KVA 100 katika kitongoji cha Wilolesi katika kijiji cha Nyamihuu ili kupunguzia mzigo wa transfoma iliyopo kuhudumia kijiji chote.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza: -

Je, Serikali haioni ni kuwakandamiza Wananchi wa Itigi kwa kuondoa Miji kwenye bei ya kuweka umeme kutoka shilingi 27,000 hadi shilingi 320,000?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI aljibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali haikandamizi mwananchi yoyote, bali inawajali na kuwaunganishia huduma ya umeme kwa gharama zenye ruzuku ndani yake. Kati ya mwaka 2008 na 2013, gharama za kuunganisha umeme zilikuwa shilingi 455,104.76 ndani ya mita 30; shilingi 1,351,883.52 ndani ya mita 70; na shilingi 2,001,421.60 ndani ya mita 120 kwa maeneo ya Mijini na Vijijini. Gharama hizi ndizo zilizokuwa zinaakisi gharama halisi za kuunganisha umeme wa njia moja.

Mheshimiwa Spika, Mwaka 2013, Serikali ilipunguza kwa kuweka ruzuku gharama za kuunganisha umeme kuwa shilingi 320,960.00 ndani ya mita 30, shilingi 515,617.52 ndani ya mita 70 na shilingi 696,669.64 ndani ya mita 120 kwa maeneo ya mijini. shilingi 177,000.00 ndani ya mita 30, shilingi 337,739.60 ndani ya mita 70 na shilingi 454,654.00 ndani ya mita 120 kwa maeneo ya vijijini.

Mheshimiwa Spika, kuanzia mwezi Januari, 2022 bei imerejea kwenye gharama za mwaka 2013 kwa maeneo ya mijini na shilingi 27,000 kwa maeneo ya vijijini. Gharama hizi zina ruzuku ya Serikali ndani yake. TANESCO inabaini eneo la miji na vijiji kwa kutumia Sheria ya Mipango Miji Namba 8 ya mwaka 2007.
MHE. BERNADETA K. MUSHASHU aliuliza: -

Je, ni vijiji vingapi havijapatiwa umeme wa REA na nini mpango wa Serikali kusambaza umeme kwenye vijiji vyote vya Mkoa wa Kagera?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bernadeta Kasabago Mushashu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Kagera una vijiji 662, ambapo kati ya hivyo, vijiji 139 havijafikiwa na miundombinu ya umeme. Vijiji vyote 139 vilivyobaki vitapatiwa umeme kupitia utekelezaji wa Mradi wa Umeme Vijijini Awamu ya Tatu – Mzunguko wa Pili unaoendelea. Mkandarasi ambaye ni Joint Venture wa kampuni za M/S JV Pomy Engineering Company Limited na Qwihaya General Enterprises Company Limited ndiyo wanaotekeleza mradi huo kwa Mkoa wa Kagera. Gharama ya mradi ni Shilingi Bilioni 34.078.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kazi za mradi zinahusisha ujenzi wa kilomita 812 za njia za umeme msongo wa kilovoti 33, ufungaji wa mashine umba 176, ujenzi wa kilomita 139 ya miundombinu ya usambazaji ya msongo wa voti 400 na uunganishaji wa wateja wa awali wapatao 3,058. Utekelezaji wa mradi umeshaanza kwa mkandarasi kukamilisha upimaji na usanifu wa kina na kuanza uagizaji wa vifaa vya utekelezaji. Mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo Desemba, 2022.
MHE. HASSAN Z. KUNGU aliuliza: -

Je, ni lini Mradi wa REA II utakamilika katika Vijiji 23 vilivyobaki vya Jimbo la Tunduru Kaskazini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Zidadu Kungu, Mbunge wa Tunduru Kaskazini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Pili ulitekelezwa na Mkandarasi LTL ambapo jumla ya vijiji 36 vya Wilaya ya Tunduru vilipatiwa umeme na mradi ulikamilika Mwaka 2015.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili katika Jimbo la Tunduru Kaskazini ambapo unatekelezwa na Mkandarasi M/S JV Guangdong Jianneng Electric Power Engineering Co. Ltd. and White City International Contractors Ltd. unalenga kupeleka umeme katika vijiji 23.

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi yupo katika maeneo mbalimbali ya mradi akiendelea na kazi za ujenzi wa miundombinu na kuunganisha wateja. Mradi unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2023.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza: -

Je, ni lini Mradi wa Umeme wa Nguvu ya Jua utaanza kutekelezwa katika Kata ya Talaga Wilayani Kishapu?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Kishapu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ujenzi wa Mradi wa Umeme wa Jua katika Kijiji cha Ngunga, Kata ya Talaga, Wilayani Kishapu unalenga kuzalisha umeme kwa kutumia jua kiasi cha megawati 150 kwa gharama za Euro milioni 115.30 ambayo itakuwa ni megawatIi 50 na Euro milioni 42 kwa awamu ya kwanza na megawati 100 kwa Euro milioni 62 kwa awamu ya pili. Fedha za awamu ya kwanza tayari zimepatikana, taratibu za kumpata Mkandarasi Mshauri na Mjenzi zipo katika hatua za mwisho. Fedha ya awamu ya pili inaendelea kutafutwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, malipo kwa ajili ya fidia kwa wananchi wa Kijiji cha Ngunga watakaoathirika na mradi, kiasi cha shilingi bilioni 1,825 kitaanza kulipwa mwishoni mwa mwezi Aprili, 2023 na Ujenzi wa Mradi huu (awamu ya kwanza) utatekelezwa kwa kipindi cha miezi kumi na nne (14) kuanzia mwezi Juni, 2023, baada ya kukamilisha taratibu za manunuzi ya wakandarasi na malipo ya fidia.
MHE. BUPE N. MWAKANG’ATA aliuliza: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kufungua vituo vingi zaidi vya kuuza gesi asilia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bupe Nelson Mwakang’ata, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiachana na usambazaji wa gesi asilia kwa kutumia bomba la kusafirisha gesi Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam, kuna vituo vitatu vya kugandamiza na kuuza gesi asilia nchini (Compressed Natural Gas (CNG) Stations) ambapo Dar es Salaam viko viwili (2) na Mtwara kipo kimoja (1). Vituo viwili vinamilikiwa na wawekezaji binafsi na kimoja ni ubia wa Serikali na Sekta Binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka 2022/2023, Serikali imempata Mkandarasi wa ujenzi wa vituo vitatu (3) vya (CNG) na kazi hiyo itaanza kabla ya mwaka huu wa fedha kwisha. Vilevile, kituo kimoja (1) kitajengwa na mwekezaji binafsi (Dangote) eneo la Mkuranga, Pwani. Aidha, Serikali imeshatoa idhini kwa kampuni binafsi 20 kujenga vituo vya kujaza gesi katika magari. Kampuni hizo zipo katika hatua mbalimbali za kupata vibali vya ujenzi.

Mheshimiwa Spika, katika hatua nyingine, Serikali imepanga kujenga vituo vya CNG katika Bohari Kuu za Serikali za Dar es Salaam na Dodoma ili kuwezesha magari ya Serikali na watu binafsi yanayoendelea kuunganishwa na mfumo wa kutumia gesi asilia kuweza kupata nishati hiyo. Taratibu za utekelezaji wa mradi huu zinakamilishwa Serikalini ili utekelezaji uanze mara moja.
MHE. NANCY H. NYALUSI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha usambazaji wa umeme katika Vijiji Nane vya Wilaya ya Mufindi ambavyo havijapata umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Nancy Hassan Nyalusi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Mufindi ina jumla ya vijiji kumi tu ambavyo havina umeme na vinapatiwa umeme kupitia Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili, kupitia Mkandarasi anayeitwa OK Electrical Services Limited. Hadi kufikia mwezi Aprili, 2023 vijiji vinane vilikuwa vimeshapatiwa umeme na vijiji viwili (2) vijulikanavyo kwa majina ya Itika na Mpangatazara bado havijapatiwa umeme. Vijiji vyote vinatarajiwa kupatiwa umeme ifikapo mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.
MHE. ALLY M. KASSINGE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itakamilisha utekelezaji wa Sera ya kupeleka umeme Vijijini kupitia Mpango wa REA III Mzunguko wa Pili?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mohamed Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mradi wa kusambaza umeme vijijini, awamu ya tatu mzunguko wa pili unaosambaza umeme vijijini vikiwemo vijiji vya Kilwa Kusini vyote, unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2023. Aidha, Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Dkt. Samia Suluhu Hassan imeongeza wigo wa mradi toka kilomita moja kwa kila kijiji na kufikia kilomita tatu (1+2) katika usambazaji wa umeme katika vijiji ili kuwafikia wananchi wengi zaidi.

Mheshimiwa Spika, awamu hii ya REA III Round II itakapokamilika hakuna kijiji ambacho kitabaki bila umeme.
MHE. KILUMBE S. NG’ENDA aliuliza: -

Je, nini matokeo ya utafiti wa mafuta uliofanyika katika Ziwa Tanganyika na lini mafuta yataanza kuchimbwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kilumbe Shabani Ng’enda, Mbunge wa Kigoma, Mjini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wa mafuta katika Ziwa Tanganyika umegawanyika katika vitalu viwili ambavyo ni Kitalu cha Kaskazini na Kusini. Kitalu cha Kaskazini kina ukubwa wa kilomita za mraba 9,430 ambapo mwaka 2015/2016, TPDC iliweza kukusanya, kuchakata na kutafsiri taarifa za uvutano wa sumaku ili kugundua maeneo yenye uwezekano wa kuwepo kwa mashapo ya kuhifadhi mafuta. Kitalu cha Kusini kina ukubwa wa kilomita za mraba 7,163 ambapo TPDC kwa kushirikiana na Mwekezaji - Kampuni ya Beach Petroleum waliweza kukusanya, kuchakata na kutafsiri taarifa za uvutano wa sumaku ili kubaini maeneo yenye uvutano na uwezekano wa kuhifadhi mafuta.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuwepo kwa viashiria vizuri vya uwepo wa mafuta katika vitalu vya Ziwa Tanganyika, matokeo ya mwisho kuhusu uwepo wa mafuta katika Ziwa hilo bado hayajapatikana kwa kuwa kazi ya utafiti bado inaendelea. Ahsante.
MHE. COSATO D. CHUMI aliuliza: -

Je, ni lini Mafinga itanufaika na Mradi wa Umeme wa Peri-Urban?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Cosato David Chumi, Mbunge wa Mafinga Mjini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, baadhi ya maeneo na Mitaa ya Mji wa Mafinga yatanufaika na Mradi wa Ujazilizi Awamu ya Pili C (Densification IIC) ambao upo katika hatua za ununuzi wa Wakandarasi. Aidha, Serikali imekamilisha uhakiki wa vitongoji visivyo na huduma ya umeme na kuandaa mradi kabambe wa kusambaza umeme katika vitongoji vyote uitwao Hamlet Electrification Project ambapo Mafinga Mjini nayo itanufaika na mradi huu. Mradi huu unatarajiwa kutekelezwa kuanzia Mwaka wa fedha wa 2023/2024 kulingana na upatikanaji wa fedha, nakushukuru.
MHE. ALLY A. J. MLAGHILA aliuliza: -

Je, ni lini umeme wa REA utafika katika Kijiji cha Ikombe – Kyela?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ally Anyigulile Jumbe Mlaghila, Mbunge wa Kyela, kama Ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Ikombe kitapata huduma ya umeme kupitia Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili unaotekelezwa na Mkandarasi M/s ETDCO Ltd. Kazi ya ujenzi wa miundombinu ya umeme katika Kijiji cha Ikombe kutoka Kijiji cha Lyulilo inatarajiwa kuanza mwezi Mei, 2023 na inatarajiwa kukamilika mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA K.n.y. MHE. TAUHIDA CASSIAN GALLOS aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kukusanya madeni ya TANESCO katika taasisi kubwa ili shirika hilo liweze kujiendesha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri napenda kujibu swali la Mheshimiwa Tauhida Cassian Gallos, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka kufikia mwezi Machi, 2023, TANESCO inadai jumla ya shilingi bilioni 244 kutoka kwa wateja wake mbalimbali wakiwemo wateja wa umma na wateja binafsi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuzuia ukuaji na kuwezesha ukusanyaji wa deni, kwa upande wa Serikali, Serikali inahakikisha inatenga na kuweka fungu la fedha za kulipia huduma hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, TANESCO imeweka mikakati ya kukusanya na kuzuia madeni kwa kuweka mita za LUKU, kuhamasisha na kufuatilia madeni na inapobidi basi kukata huduma ya umeme kwa mteja mwenye deni kubwa na sugu ili liweze kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme wa REA kwenye Vijiji 23 Wilayani Mkalama?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini, Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili, katika Wilaya ya Mkalama unatekelezwa na Mkandarasi CRJE – CTCE Consortium. Mradi unalenga kupeleka umeme katika vijiji vyote 25 vya Wilaya ya Mkalama ambavyo havina umeme na Mkandarasi yupo katika eneo la site akiendelea kuwasha umeme.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla, mradi huu wa kusambaza umeme katika Wilaya ya Mkalama unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Disemba, 2023, nakushukuru.
MHE. ESTHER E. MALLEKO aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika Vijiji na Vitongoji vya Mkoa wa Kilimanjaro ambavyo havina huduma ya umeme?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Esther Edwin Malleko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimwa Naibu Spika, Mkoa wa Kilimanjaro una jumla ya vijiji 519 ambapo mpaka sasa vijiji 11 tu havina umeme. Vijiji hivi vimepangwa kupatiwa umeme kupitia Mradi wa REA, awamu ya tatu, mzunguko wa pili, ambao unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kilimanjaro una vitongoji 2,260 na kati ya hivyo, vitongoji 286 tu ndiyo havina umeme. Vitongoji hivyo vitaendelea kupatiwa umeme kupitia Miradi ya Ujazilizi kwa kadri fedha zitakavyopatikana, ahsante.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kupeleka umeme katika Kata ya Mletele Wilayani Songea?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Kata ya Mletele katika Manispaa ya Songea ina jumla ya mitaa sita ambayo ni Mletele, Makemba, Liumbu, Nonganonga, Mdundiko na Mji Mwema. Mitaa mitano ya Mletele, Makemba, Liumbu, Nonganonga na Mdundiko tayari ina umeme. Mtaa wa Mji Mwema tu ndiyo bado haujafikiwa na umeme.

Mheshimiwa Spika, mtaa huu tayari umefanyiwa tathmini na utapata umeme kwa kuweka miundombinu itakayogharimu shilingi 115,767,782.60 katika Mwaka wa Fedha 2023/2024. Nashukuru.
MHE. YAHAYA O. MASSARE aliuliza: -

Je, ni lini ukarabati utafanywa katika njia ya umeme kutoka kituo kikubwa kuelekea Ikungi, Manyoni, Itigi, Mitundu hadi Mwamagembe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yahaya Omary Massare, Mbunge wa Manyoni Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Singida umeunganishwa na Gridi ya Taifa kutoka katika kituo cha kupoza umeme kilichopo Mkoani Dodoma kupitia njia ya kusafirisha umeme za msongo wa kilovolti 220 na 400 hadi kituo cha kupoza umeme cha Singida. Kwa kutumia msongo huo mkubwa, Serikali kulingana na upatikanaji wa fedha imepanga kujenga kituo kikubwa cha kupoza umeme Wilayani Manyoni ili kuondoa changamoto za umeme kusafiri umbali mrefu.

Mheshimiwa Spika, matengenezo ya njia ya kusafirisha umeme ya msongo wa kilovolti 33 kutoka kituo kikubwa cha kupoza umeme cha Singida kuelekea Manyoni, Itigi, Mitundu hadi Mwamagembe tayari yanaendelea na katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imetenga kiasi cha shilingi 471,000,000.00 kwa ajili ya matengenezo ya njia hiyo. Vilevile mkandarasi wa njia ya reli ya SGR atakapomaliza ujenzi eneo la Kintinku, TANESCO itaunganisha njia ya umeme kutoka Wilaya ya Bahi kwenda Manyoni, hivyo kuimarisha upatikanaji wa umeme katika maeneo hayo.
MHE. NDAISABA G. RUHORO aliuliza: -

Je, lini Mradi wa Bwawa la kufua umeme wa RUSUMO utazinduliwa ili kuondoa tatizo la kukatika kwa umeme Ngara?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swala la Mheshimiwa Ndaisaba George Ruhoro, Mbunge wa Ngara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kufua umeme wa Rusumo wa Megawati 80 wa nchi tatu za Tanzania, Burundi na Rwanda ambazo zitagawanywa sawa, umefikia asilimia 99 na utaanza kufanya kazi mwezi Juni, 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, mashine tatu za kuzalisha umeme zitawashwa kwa mashine moja kila mwezi kuanzia mwezi wa Juni na hivyo tunatarajia kuuzindua baada ya mwezi wa saba baada ya kuwashwa kwa mashine zote tatu kukamilika, nashukuru.
MHE. KAVEJURU E. FELIX aliuliza: -

Je, lini mradi wa kuunganisha umeme wa Gridi ya Taifa kutoka Nyakanazi hadi Kigoma utaanza?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Kavejuru Eliadory Felix, Mbunge wa Buhigwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni habari njema kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, tayari imeunganisha Mkoa wa Kigoma katika Gridi ya Taifa tangu mwezi Septemba, 2022 kwa kuanzia Wilaya za Kakonko, Kibondo, Kasulu na Buhigwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hatua nyingine kubwa zaidi, hadi kufika mwezi Aprili, 2023, Mkandarasi aitwaye TATA Projects Ltd. amefikia 53% ya utekelezaji wa mradi wa kuunganisha Mkoa wa Kigoma katika Gridi ya Taifa kwa kujenga njia ya kusafirisha umeme yenye msongo wa kilovolti 400 toka Nyakanazi (Biharamulo) mpaka Kidahwe (Kigoma) kwa urefu wa kilometa
280. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Januari, 2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ya ziada ambayo Serikali inaitafutia fedha ni njia ya kusafirisha umeme (kilovoti 220) ya kutoka Kasulu hadi Buhigwe pamoja na Kituo cha Kupooza Umeme cha Kasulu ambapo thamani ya mradi ni Dola za Kimarekani milioni 20.5. Pia njia ya kusafirisha umeme (kilovolti 220) kutoka Buhigwe hadi Kigoma na Kituo cha Kupooza Umeme cha Buhigwe kwa thamani ya mradi ya dola milioni 19.8 za Kimarekani, ahsante.
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA aliuliza: -

Je, lini Serikali itamaliza tatizo la umeme Mkoani Mtwara hususani Wilaya ya Masasi na Jimbo la Lulindi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Masasi inapata umeme kutoka katika Kituo cha Kuzalisha Umeme kwa Kutumia Gesi cha Mtwara chenye uwezo wa megawati 30.4 na pia umeme wa Gridi ya Taifa kupitia njia ya msongo wa kilovoti 33 kutokea Songea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya umeme Mkoani Mtwara, Wilayani Masasi ikiwemo Jimbo la Lulindi inatokana na Umeme mdogo usiotosheleza (low voltage) kwenye baadhi ya maeneo ya Wilaya hiyo kwa sababu ya umeme kusafiri umbali mrefu, uchakavu wa miundombinu hasa nguzo na vikombe pamoja na uharibifu kwenye miundombinu ya njia ya msongo wa kilovoti 132 unaotokana na watoto kupiga manati vikombe katika baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa tatizo hili Serikali kupitia TANESCO imetenga shilingi bilioni mbili ili kujenga njia ya kutoka Nanganga hadi Masasi. Aidha, ufungaji wa Auto Voltage Regulator (AVR) mpya yenye ukubwa wa MVA 20 kati ya Tunduru na Namtumbo unaendelea ili kuwezesha umeme wa kutosha kutoka Ruvuma kufika Masasi na maeneo ya jirani. Pia, kwa kutumia Shilingi Milioni 600 Serikali inaendelea kubadili vikombe vilivyopasuka na kuweka vya plastiki na nguzo za miti zilizooza zinabadilishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuwa na ufumbuzi wa kudumu wa tatizo la umeme katika Mkoa wa Mtwara, Serikali imepanga kuunganisha Mkoa wote na Gridi ya Taifa kupitia miradi miwili ya Gridi Imara ambayo ipo katika hatua za utekelezaji. Miradi hii ni ujenzi wa njia kuu ya umeme ya msongo wa kilovoti 220 kutoka Songea hadi Tunduru na kutoka Tunduru hadi Masasi. Ahsante.
MHE. DKT. ALICE K. KAIJAGE K.n.y. MHE. TWAHA A. MPEMBENWE aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa Ofisi ya Wilaya ya TANESCO – Kibiti?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Twaha Ally Mpembenwe, Mbunge wa Kibiti kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa umahususi na umuhimu wa Wilaya ya TANESCO Kibiti, TANESCO inafanya tathmini ya gharama kuangalia namna ya kujenga jengo lake la ofisi ili kuepuka kuendelea na ofisi iliyopo sasa ambayo ni ya kupanga.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, kutokana na maendeleo makubwa ya teknolojia, kwa sasa huduma nyingi zinatolewa kwa njia ya mtandao. Aidha, programu kama vile NIKONEKT, NIHUDUMIE, kununua umeme (LUKU) na nyinginezo zimeanzishwa ili kurahisisha utoaji wa huduma kwa wateja bila kulazimika kwenda ofisi za TANESCO. Aidha, pamoja na faida nyingine programu hizi zimesaidia kuondoa vishoka waliokuwa wanawalaghai wateja katika ofisi za TANESCO.

Mheshimiwa Spika, shirika limeelekeza fedha nyingi katika kuanzisha na kuboresha huduma zinazotolewa kwa njia ya mtandao. Sambamba na hili, shirika linaendelea kuanzisha viunga/ofisi ndogo zitakazokuwa karibu zaidi na wananchi ili kuwahudumia kwa haraka kwa huduma chache ambazo hazipatikani kwa mtandao kwa sasa. Katika Wilaya ya Kibiti, TANESCO imeanzisha viunga viwili katika maeneo ya Hanga na Bungu ili kusogeza huduma kwa wateja. Ahsante.
MHE. MOHAMED L. MONNI aliuliza: -

Je, lini Serikali itakamilisha kusambaza umeme katika Vijiji vya Chemba?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mohamed Lujuo Monni, Mbunge wa Chemba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) inatekeleza Mradi Kabambe wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu Mzunguko wa Pili ambapo, vijiji vyote ambavyo havina umeme Tanzania Bara vitafikiwa na huduma ya umeme.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo la Chemba, Mkandarasi M/s Sagemcom Limited alipewa jumla ya vijiji 59 ambavyo havikuwa na umeme. Hadi kufikia tarehe 15 Agosti, 2023, vijiji 47 vimeshawashiwa umeme na vijiji 12 viko kwenye hatua mbalimbali za utekelezaji na vitakamilika kabla ya mkataba wa mkandarasi kuisha tarehe 31 Oktoba, 2023.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID aliuliza:-

Je, ahadi ya Serikali ya kusambaza umeme wa REA III katika vijiji 48 vya Jimbo la Same Magharibi na vitongoji vyake imefikia wapi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. David Mathayo David, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Same, Vijiji 91 kati ya 100 tayari vimepelekewa umeme na vijiji tisa vilivyobaki vitapelekewa umeme ifikapo mwezi Desemba, 2023.

Mheshimiwa Spika, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Serikali imepanga kuanza ujenzi wa miundombinu ya kusambaza umeme katika vitongoji 2,034 nchini kwa gharama ya shilingi bilioni 377.05 ambapo vitongoji 15 katika Jimbo la Same Magharibi vitapelekewa umeme. Serikali itaendelea kupeleka umeme kwenye vitongoji 162 vilivyobaki kulingana na upatikanaji wa rasilimali fedha, nakushukuru.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO aliuliza:-

Je, lini Serikali itapeleka umeme katika Kata za Lagana, Itilima na Bunambiyu Wilayani Kishapu?
NAIBU WAZIRI NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Nyangindu Butondo, Mbunge wa Kishapu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkandarasi M/S SUMA JKT anayetekeleza mradi wa REA III Round II katika Wilaya ya Kishapu ana jumla ya vijiji 51 katika mkataba wake, vikiwemo vijiji vya Kata za Lagana, Itilima na Bunambiyu Wilayani. Mkandarasi kwa sasa anaendelea na utekelezaji wa mradi ambapo ameshawasha umeme katika vijiji 13 kati ya 51 sawa na asilimia 25.5. Aidha, kati ya vijiji 13 vilivyowashwa, vijiji vitano ni vya Kata ya Itilima. Mkandarasi anaendelea na ujenzi katika vijiji 38 vilivyobakia vikiwemo vijiji vitano vya Kata ya Lagana, vijiji vitatu vya Kata ya Itilima na vijiji viwili vya Kata ya Bunambiyu ambavyo vinatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2023.

Mheshimiwa Spika, ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa wakati, Serikali imemfungulia Mkandarasi Hati ya Muamana (LC) ili aweze kuhakikisha anaongeza kasi ya kufanya kazi na kuimaliza mwezi Desemba, 2023, nakushukuru.
MHE. DEO K. SANGA aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapitia upya uhalisia wa malipo ya umeme kwa Vijiji vya Mkolango, Kiumba, Ikwete na Malombwe ambapo walilipia kwa bei ya Mjini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Deo Kasenyenda Sanga, Mbunge wa Makambako, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Vijiji vya Ikwete na Mkolango, wananchi wote wa maeneo hayo wanalipia gharama ya shilingi 27,000 kwa ajili ya kuunganishiwa umeme. Aidha, Vijiji vya Malombwe na Kihumba ni miongoni mwa vijiji vyenye sura ya Vijiji-Miji ambavyo kwa tathmini ya awali, vilionekana vinastahili kulipia shilinigi 320,960 kama garama ya kuunganishiwa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kubaini changamoto katika tathmini ya awali, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kufanya tathmini ya maeneo yote yenye sura ya Vijiji-Miji yakiwemo maeneo ya Malombwe na Kiumba ili kuyapatia suluhisho la gharama za kuunganishiwa umeme. Serikali inaendelea kuomba wananchi wa maeneo hayo wawe na subira wakati suala hili linashughulikiwa.
MHE. TUNZA I. MALAPO K.n.y MHE. STELLA S. FIYAO aliuliza:-

Je, kuna mkakati gani wa kuhakikisha Vijiji vyote vya Mkoa wa Songwe vinapatiwa umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Songwe una jumla ya vijiji 307 ambapo hadi kufikia tarehe 31 Mei 2023, vijiji 240 vilikua tayari vimepatiwa umeme, Vijiji 67 vilivyosalia viko kwenye mkataba wa Mkandarasi M/s Derm Electrics Ltd anayetekeleza mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu III Mzunguko wa II katika Mkoa wa Songwe. Kazi za ujenzi wa miundombinu na kuunganisha wateja katika vijiji hivyo inaendelea na mradi unatarajiwa kukamilika Desemba, 2023, nakushukuru.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA aliuliza:-

Je, ni kwa nini bei ya kuunganisha umeme katika Kijiji cha Lwamgasa ni shilingi 321,000 tofauti na vijiji vingine?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Magessa Tumaini, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa kutoka TAMISEMI, eneo la Lwamgasa linatambuliwa kama Mji Mdogo na hivyo malipo ya gharama ya kuunganisha umeme iliwekwa 320,960 kwa vile panakidhi mwonekano wa mji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imepokea maombi mengi kutoka kwa wakazi wa maeneo ya vijiji miji wanaotozwa shilingi 320,960 kama gharama za kuunganisha umeme ndani ya mita 30 iwe 27,000. Kijiji cha Lwamgasa ni miongoni mwa vijiji miji hivi. Kwa sasa, uchambuzi bado unaendelea ili kubaini uhalisia wa maeneo hayo. Uchambuzi ukikamilika gharama halisi stahiki zitatolewa, nashukuru.
MHE. FESTO R. SANGA aliuliza:-

Je, lini wananchi waliopitiwa na ujenzi wa Bwawa la Umeme la Mto Lumakali Makete watalipwa fidia?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Festo Richard Sanga, Mbunge wa Makete, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa ujenzi wa Bwawa la Mto Lumakali unalenga kuzalisha umeme wa MW 222 kwa kutumia maji ya Mto Lumakali mkoani Njombe na unahusisha pia ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme yenye msongo wa kV 220 yenye urefu wa kilometa 65 kutoka kwenye mitambo hadi Kituo cha Kupoza Umeme cha Iganjo mkoani Mbeya. Gharama za ujenzi wa kituo cha kuzalisha umeme ni takribani shilingi trilioni 1.42 na ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme ni takribani shilingi bilioni 50.3.

Mheshimiwa Naibu Spika, tathmini ya awali ya mali za wananchi wanaopisha Mradi wa Ujenzi Bwawa la Umeme la Mto Lumakali imekamilika na Serikali imetenga fedha katika mwaka wa fedha 2023/2024 kwa ajili ya kuanza malipo ya fidia kwa wananchi hao. Kwa sasa kazi ya uhakiki inaendelea kwa mwezi Juni, 2023 na baada ya kazi hiyo kukamilika malipo ya fidia kwa wananchi wanaopisha mradi yanatarajiwa kuanza kulipwa kuanzia mwezi Julai, 2023, nashukuru.
MHE. JAFARI W. CHEGE aliuliza: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha umeme unafika kwenye vitongoji vyote nchini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Jafari Wambura Chege, Mbunge wa Rorya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishati Vijijini (REA) imekamilisha uhakiki wa vitongoji 36,101 visivyokuwa na huduma ya umeme na kuandaa mradi kabambe wa kusambaza umeme katika vitongoji vyote uliopewa jina Hamlet Electrification Project (HEP) vikiwemo vijiji 262 vya Wilaya ya Rorya. Mradi huu utagharimu takribani shilingi 6,700,000,000,000.

Mheshimiwa Spika, Serikali inakamilisha mipango ya upatikanaji wa fedha hiyo na mradi huu unatarajiwa kutekelezwa ndani ya miaka mitano kuanzia mwaka wa fedha 2024. Aidha, katika mwaka wa fedha 2023/2024 Jimbo la Rorya litapatiwa fedha kutoka REA ya kufikisha umeme katika vitongoji 15 vya kuanzia, nashukuru.
MHE. MAIMUNA A. PATHAN aliuliza:-

Je, ni lini tatizo la kukatika umeme mara kwa mara Mkoani Lindi litakwisha?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Maimuna Ahmad Pathan, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Lindi unapata umeme kutoka katika vyanzo viwili ambavyo ni mitambo ya kufua umeme wa gesi iliyopo Mtwara na Lindi (Somanga).

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi kifupi (siku 90), Serikali imeandaa mkakati wa kuongeza upatikanaji wa umeme mikoa ya Lindi na Mtwara kwa kupeleka jenereta ya megawati 20, kufanya ukarabati wa miundombinu ya kusambaza umeme na kufunga vifaa vinne vya kuzima na kuwasha umeme (Autoclosers) kwenye njia mchepuko. Utekelezaji wa Mipango hii ulianza mwezi Mei, 2023.

Mheshimiwa Naibu Spika, mikakati mitatu ya muda mrefu ni kujenga njia yenye msongo wa kilovoti 220 Songea – Tunduma (mradi huu ulianza mwezi Machi, 2023 na utachukua miezi 18). Kujenga njia yenye msongo wa kilovoti 220 Tunduru – Masasi, Mkandarasi atakabidhiwa eneo la mradi mwezi Juni, 2023. Ujenzi wa njia yenye msongo wa kilovoti 220 Masasi - Mahumbika ambayo upembuzi utaanza mwaka wa fedha 2023/2024.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika hatua nyingine kubwa, Serikali inaendelea na mazungumzo na Shirika la Maendeleo la Japan (JICA) juu ya ujenzi wa kituo kikubwa kitakachozalisha Megawati 300 Mkoani Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, miradi hii itakapokamilika, hali ya umeme katika mikoa ya Mtwara na Lindi itaimarika sana.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza: -

Je, lini ujenzi wa KV 400 kutoka Iringa, Mbeya, Tunduma hadi Sumbawanga utaanza pamoja na kulipa wananchi waliopitiwa na laini hiyo?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa ujenzi wa njia ya kusafirisha umeme wa msongo wa KV 400 yenye urefu wa kilometa 620 kutoka Iringa hadi Sumbawanga kupitia Mbeya na Tunduma unatarajiwa kuanza mwezi Juni, 2023 na kukamilika mwezi Septemba, 2025. Mradi huu unalenga kuunganisha Gridi ya Taifa na Nchi za Kusini mwa Afrika (Southern African Power Pool) na utagharimu jumla ya shilingi 1,380,000,000,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari imetoa shilingi bilioni 16.43 kwa ajili ya malipo ya fidia kwa wananchi 6,500 wanaopisha mradi na kazi ya ulipaji fidia imekamilika kwa awamu ya kwanza ambapo wananchi 4,750 wamepokea shilingi bilioni 13.67 na maandalizi ya awamu ya pili yanaendelea na malipo yanatarajiwa kufanyika ifikapo Julai, 2023.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA aliuliza:-

Je, lini zoezi la kufikisha umeme katika vitongoji, vijiji na mitaa ambayo haina umeme litakamilika Wilayani Kakonko?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Aloyce John Kamamba, Mbunge wa Buyungu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili ambapo vijiji vyote visivyokuwa na umeme vitafikiwa na huduma hiyo. Aidha, vijiji saba tu vya Wilaya ya Kakonko visivyokuwa na umeme vitakamilika kuwashiwa umeme ifikapo tarehe 30 Juni, 2023.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekamilisha uhakiki wa vitongoji 36,101 visivyo na huduma ya umeme na kuandaa mradi kabambe wa kusambaza umeme katika vitongoji vyote unaoitwa Hamlet Electrification Project (HEP) vikiwemo vitongoji 196 vya Wilaya ya Kakonko. Mradi huu utatekelezwa kuanzia mwaka wa fedha 2024/2025. Kwa mwaka 2023/2024 Jimbo la Buyungu Wilayani Kakonko litapatiwa fedha kwa ajili ya kupeleka umeme katika vitongoji 15 vya kuanzia, nakushukuru.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI aliuliza: -

Je, kuna mpango gani wa kupeleka nishati ya gesi asilia katika vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro ili kupunguza matumizi ya kuni?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Prof. Patrick Alois Ndakidemi, Mbunge wa Moshi Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, gesi asilia inaweza kusafirishwa kwa njia ya mabomba au kwa njia ya mitungi/tanki inayobebwa na malori/treni/meli ambapo gesi asilia inakuwa katika hali ya gesi iliyogandamizwa (Compressed Natural Gas – CNG) ama kimiminika (Liquefied Natural Gas – LNG). Hadi sasa, gesi asilia inachimbwa Mtwara na hivyo maeneo yaliyounganishwa na kuweza kutumia nishati ya gesi asilia ni yale yanayopitiwa na miundombinu ya mabomba ya kusafirishia gesi ambayo ni Mikoa wa Mtwara, Lindi, Pwani na Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Bomba la Kusafirisha Gesi Asilia kwenda Mombasa Nchini Kenya kupitia Mkoani Tanga, ni moja ya miradi inayotoa fursa ya kuunganisha Mikoa ya Kaskazini na gesi asilia ikiwemo Kilimanjaro kwa kuweka toleo katika eneo la Segera (Tanga). Mradi huu wa bomba bado unafanyiwa kazi Serikalini, utakapokamilika gesi asilia itaweza kufikishwa Mkoani Kilimanjaro, vikiwemo vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro na katika maeneo mengine mkoani humo na mikoa ya jirani, nakushukuru.
MHE. FLATEI G. MASSAY aliuliza:-

Je, lini Serikali itakamilisha usambazaji wa umeme wa REA katika Kata na Vijiji 23 vya Jimbo la Mbulu Vijijini?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati napenda kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Gregory Massay, Mbunge wa Mbulu Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza mradi wa kusambaza umeme vijijini awamu ya tatu mzunguko wa II ambapo vijiji vyote visivyokuwa na umeme vitafikiwa na huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, Mradi huu unahudumia vijiji 45 vilivyopo katika Jimbo la Mbulu Vijijini, ambapo kati ya hivyo, vjijiji 15 vimekwishawashiwa umeme na vijiji 30 kazi mbalimbali zinaendelea. Mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2023. Nakushukuru.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha zoezi la kuwasha umeme kwenye vijiji vilivyosalia katika Jimbo la Momba?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Condester Michael Sichalwe, Mbunge wa Momba, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatekeleza Mradi wa Kusambaza Umeme Vijijini Awamu ya Tatu, Mzunguko wa Pili ambapo vijiji vyote visivyo na umeme vitafikiwa na huduma ya umeme. Mradi huu unahudumia vijiji 42 vilivyosalia katika Jimbo la Momba ambapo kati ya hivyo vijiji 22 vimekwishawashiwa umeme na vijiji 20 kazi mbalimbali zinaendelea. Mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Disemba, 2023. Nakushukuru.
MHE. ANTON A. MWANTONA aliuliza:-

Je, lini Serikali itapeleka Umeme wa REA katika vijiji na vitongoji ambavyo vimeshawekewa nguzo Jimbo la Rungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Rungwe, mkandarasi M/S State Grid Ltd. anakamilisha maandalizi ya vifaa vya ujenzi wa maeneo yaliyobaki na kazi zinatarajiwa kuanza tarehe 1 Julai, 2023 na kukamilika mwezi Oktoba, 2023. Pamoja na miradi mingine katika bajeti ya mwaka 2023/2024, kila Jimbo limetengewa bajeti ya kupelekewa umeme katika vitongoji 15 vya kuanzia wakati maandalizi ya mradi wa Hamlet Electrification Project (HEP) unaotarajiwa kuanza mwaka 2024/2025 yanakamilika, nakushukuru.
MHE. ORAN M. NJEZA aliuliza:-

Je, ni lini wananchi wa Wilaya ya Mbeya waliopisha mradi wa njia kuu ya kusafirisha umeme mkubwa wa Kilovolti 400 watalipwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia TANESCO inaendelea na maandalizi ya ujenzi wa mradi wa njia ya kusafirisha umeme mkubwa wenye msongo wa kilovoti 400 kutoka Iringa kupitia Mbeya, Tunduma hadi Sumbawanga yenye urefu wa kilomita 616. Mradi huu pia unahusisha ujenzi wa Vituo vya Kupoza Umeme vya Iringa, Kisada, Mbeya, Tunduma na Sumbawanga pamoja na ujenzi wa kilomita nne za njia ya umeme msongo wa kilovoti 400 kwenda kwenye mpaka wa Tanzania na Zambia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uthamini unafanywa na TANESCO kwa kushirikiana na Wathamini wateule wa Wilaya za Iringa, Mufindi, Mafinga, Mbarali, Mbeya, Jiji la Mbeya, Mbozi, Tunduma, Momba na Sumbawanga ambapo katika maeneo hayo mradi unapita. Hadi kufikia Mwezi Aprili, 2022, majedwali ya fidia ya Halmashauri za Iringa, Mufindi, Mafinga, Momba na Mbarali tayari yameshaidhinishwa na Mthamini Mkuu wa Serikali na kukabidhiwa TANESCO kwa ajili ya kuanza maandalizi ya malipo. Majedwali ya Wilaya za Mbeya, Halmashauri ya Jiji la Mbeya, Mbozi, Tunduma na Sumbawanga yapo katika hatua za mwisho za ukamilishwaji. Fidia hizi zinatarajia kuanza kulipwa mwaka wa fedha 2022/2023.
MHE. JESCA D. KISHOA aliuliza:-

Je, Serikali imejipangaje kuingia mikataba mipya isiyo na dosari kwani Mwaka 2024 ndio mwisho wa mkataba wa Songas?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca David Kishoa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkataba kati ya Serikali na Kampuni ya Songas utaisha muda wake mwezi Julai, 2024. Ili kuhakikisha kwamba Serikali inakuwa na mkataba usiokuwa na dosari, Serikali haitaongeza muda wa mkataba utakaoishia mwezi Julai, 2024. Badada yake, Serikali itajadili mkataba mpya na iwapo pande zote zitakubaliana, mkataba mpya wenye tija kwa Taifa na usiokuwa na dosari utasainiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tayari Serikali kupitia TANESCO imeunda timu ya kupitia masuala ya msingi ya kuzingatiwa kwenye mkataba mpya kwa ajili ya maslahi kwa Taifa.
MHE. STELLA S. FIYAO aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango wa kuhakikisha vijiji vyote vya Mkoa wa Songwe vinapata umeme wa REA?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stella Simon Fiyao, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mkoa wa Songwe una jumla ya vijiji 307; vijiji 180 vina umeme na vijiji 127 havijafikiwa na miundombinu ya umeme. Vijiji hivyo 127 ambavyo havijafikiwa na miundombinu ya umeme vinanufaika kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili unaoendelea. Utekelezaji wa mradi unaendelea na Mkandarasi Derm Electrics ndiye anayetekeleza mradi kwa kipindi cha miezi kumi na nane kwa gharama ya shilingi bilioni 11.23. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Desemba, 2022.
MHE. GEORGE N. MALIMA aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la kukatika kwa umeme katika Mji wa Mpwapwa?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, awali Mji wa Mpwapwa pamoja na maeneo ya Wilaya za Mpwapwa, Kibaigwa na Kongwa zilikuwa zinapata huduma ya umeme kupitia njia ya ya umeme ya Mpunguzi yenye msongo wa kilovoti 33 na urefu wa kilometa 660.4 kutoka katika kituo cha kupoza umeme cha Zuzu, Dodoma Mjini. Kutokana na urefu na uchakavu wa njia hiyo, kulikuwepo na tatizo la kupungua kwa nguvu za umeme yaani low voltage katika maeneo ya Wilaya za Kongwa na Mpwapwa. Hata hivyo, Serikali kupitia TANESCO ilikamilisha ufungaji wa kifaa kiitwacho AVR yaani Automatic Voltage Regulator katika eneo la Kibaigwa na hivyo kufanikiwa kupunguza tatizo hilo.

Mheshimiwa Spika, tarehe 3 Agosti, 2021 Serikali kupitia TANESCO ilikamilisha ujenzi wa njia mpya ya kusambaza umeme ya msongo wa kilovoti 33 inayohudumia maeneo ya Wilaya za Kongwa na Mpwapwa. Kukamilika kwa ujenzi wa njia hii kumefanya njia iliyokuwepo awali kuendelea kuhudumia maeneo ya Kibaigwa pekee na hivyo kufanya maeneo ya Kongwa na Mpwapwa kuwa na umeme wa kutosha.

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia TANESCO inaendelea kuimarisha hali ya upatikanaji wa umeme nchini ikiwemo Wilaya ya Mpwapwa na katika mwaka wa fedha 2022/2023 TANESCO itatengewa shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kufanya matengenezo na kuboresha nguvu za umeme katika njia chepushi za umeme yaani spur lines ikiwa ni pamoja na kubadilisha nguzo za miti kuweka za zege hasa katika maeneo korofi, kubadilisha vikombe na nyaya zilizochakaa pamoja na kufunga vikata umeme vinavyojiendesha vyenyewe yaani auto reclosers. (Makofi)
MHE. MICHAEL M. KEMBAKI aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapeleka umeme kwenye mitaa 61 katika Mji wa Tarime?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Michael Mwita Kembaki, Mbunge wa Tarime Mjini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mamlaka ya Mji wa Tarime ina jumla ya mitaa 81. Kati ya Mitaa hiyo, Mitaa 53 ina umeme na Mitaa 28 haijapata huduma ya umeme. Mitaa minne ya Nyamiobo, Kogesenda, Itununu, na Nguku itapatiwa huduma ya umeme kupitia Mradi wa ujazilizi (Densification 2C) unaotarajiwa kuanza mwezi Agosti, 2022. Mitaa mingine 24 iliyobaki inaendelea kupatiwa huduma ya umeme na TANESCO kadri ya upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kutafuta fedha kwa ajili ya kufikisha umeme katika mitaa yote katika kipindi kifupi kijacho.
MHE. IDDI K. IDDI aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanzisha Mkoa wa TANESCO katika Wilaya ya Kahama na kujenga Ofisi ya TANESCO Halmashauri?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, TANESCO imekuwa ikifungua Ofisi za Mikoa na Wilaya katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuzingatia mahitaji na vigezo muhimu ikiwa ni pamoja na Wilaya, ongezeko la wateja, ukubwa wa mtandao na miundombinu ya umeme katika maeneo husika. Katika Halmashauri ya Mji wa Kahama ipo Ofisi ya TANESCO ya Wilaya ya Kahama inayotoa huduma kwa wananchi wa Mji wa Kahama pamoja na Halmashauri za Msalala na Ushetu.

Mheshimiwa Spika, katika hatua ya kusogeza huduma zaidi kwa wananchi, TANESCO imefungua Ofisi ndogo yaani Sub Offices katika maeneo ya Nyamilangano, Ilogi na Isaka. TANESCO inaendelea kuongeza Ofisi ndogo nyingine katika maeneo ya Segese, Bulungwa, Bulige na Chambo pamoja na kuongeza watumishi, magari na majengo. TANESCO inaendelea na tathmini ya mahitaji na vigezo kwa ajili ya kufungua Ofisi ngazi ya Mkoa katika Mji wa Kahama.
MHE. CECIL D. MWAMBE aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaviunganishia umeme vijiji vya Jimbo la Ndanda vilivyopitiwa na nguzo za umeme wa msongo wa 33KV kuelekea Masasi?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecil David Mwambe, Mbunge wa Ndanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo la Ndanda lina jumla ya kata 16 na vijiji 69, vijiji 33 vina umeme na 36 bado havijapata umeme vikiwemo vijiji vya Mkungu, Chipite, Mkang’u, Mumburu B, Muongozo, Mdenga na Mbemba vinavyopitiwa na njia ya umeme ya msongo wa kilovoti 33 kutoka kituo cha kupoza umeme cha Mahumbika kuelekea Masasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji vyote 36 ambavyo havina umeme katika Jimbo la Ndanda vinapatiwa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa pili unaotekelezwa na Mkandarasi M/s Namis Corporate Engineers and Contractors. Mradi huu unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2022.
MHE. ALLY A. J. M. JUMBE K.n.y. MHE. ANTON A. MWANTONA aliuliza: -

Je, ni lini Mradi wa REA II wenye vijiji 25 na REA III wenye vijiji 33 utakamilika katika Jimbo la Rungwe?
NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Rungwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, vijiji takribani 25 vilivyokuwa vinatekelezwa chini ya Mradi wa REA II vimeshafanyiwa uhakiki ili kujua upungufu ambao haujafanyiwa kazi. Marekebisho ya upungufu uliobainika katika vijiji hivyo utarekebishwa ndani ya miezi mitatu kuanzia mwezi Julai, 2022. Kazi hizo zitatekelezwa na Mkandarasi M/S ETDCO.

Mheshimiwa Naibu S[pika, Mradi wa REA III Mzunguko wa II ambao unapeleka umeme katika vijiji 33 vya Wilaya ya Rungwe unatarajiwa kukamilika ifikapo mwezi Desemba, 2022. Kwa sasa, Mkandarasi M/S Electrical Transmission and Distribution Construction and Maintenance Co. LTD anaendelea na kazi ya kupeleka umeme katika vijiji hivyo.