Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Stephen Lujwahuka Byabato (5 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia hoja hii ya Mpango. Niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba Wizara ya Nishati maoni yao na mapendekezo tumeyachukua na tutayafanyia kazi kwa upana wake. Niongelee tu kwenye maeneo machache mengine ni ya kuweka taarifa sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza kwenye gesi asilia. Kama tulivyosema juzi Serikali imeipa mtaji TPDC wa dola bilioni 1.193. Kwa kubadilisha deni la bomba la gesi kuwa sasa pesa ambayo TPDC inaweza ikaitumia. Kwa hiyo hatuna wasiwasi na tunakoelekea kwamba TPDC itaweza kukopesheka na kufanya biashara katika mazingira ambayo itakuwa na bargaining power za kuweza kupata mikopo yenye riba nafuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili tayari mikataba ya interest MOU zimesainiwa kati ya Tanzania na Uganda, Tanzania na Kenya, wenzetu wa Malawi na Rwanda wameonesha interest, kwa hiyo tukitoa gesi hii Dar es Salaam na Mtwara kupeleka Uganda hii Mikoa yote ya katikati itapata tukipeleka Kenya Mikoa ya katikati itapata kwa hiyo humu ndani tutaisambaza vya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ambalo nimeona nilisemee kidogo ni eneo la idadi ya vijiji vyenye umeme na visivyokuwa na umeme. Ukurasa wa 32 wa Mpango umeeleza taarifa na ni taarifa sahihi na naomba niseme kwa sasa. Vijiji tulivyonavyo kwa mujibu wa takwimu za TAMISEMI ni 12,345, kwa mujibu wa taarifa za TAMISEMI na kwenye mpango imeandikwa hivyo. Vijiji vyenye umeme mpaka kufikia Tarehe 31/10/2022 ni 9,163, Vijiji ambavyo bado ambavyo vyote viko kwenye REA III round II ni Vijiji 3,182 ambavyo mikataba yake inaendelea kwenye maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya takwimu ilitokea kwenye mazingira tuliyokuwa tunafanyia kazi. Huko nyuma kuna vitongoji vikubwa ambavyo vilipewa umeme na wenzetu wakavihesabu kama vijiji. Sasa vimeondolewa kwenye idadi ili tubakie na vijiji halisia na Waheshimiwa Wabunge tunafahamu kwenye maeneo yetu, maeneo ambayo tumeweka umeme kwenye vitongoji lakini vilihesabiwa kama vijiji. Sasa taarifa sahihi ni hii Vijiji 12,345, Vijiji 9163 tayari umeme na Vijiji 3182 umeme bado lakini vina mikataba vyote na vinafanyiwa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Tatu ni kwenye uhakika wa umeme na wenye gharama nafuu. Mpango wetu umeelaza vizuri kabisa kwenye ukurasa wa 18, ukurasa 32 na kiambatisho C ukurasa wa 1- 3, umeeleza miradi mingi sana ya uzalishaji na usafirishaji wa umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mchangiaji alisema hata mpango wa kutoa umeme Mwalimu Nyerere kuuleta Chalinze haupo. Ukurasa wa 33 umeeleza vizuri kabisa kwamba tunatoa umeme Mwalimu Nyerere na tutauleta Chalinze na kazi inaendelea tunatarajia ikamilike mwaka unaokuja na miradi ya kutoka Chalinze kuja Dodoma, kutoka Chalinze kwenda Mwalimu Nyerere yote imeelezwa kwenye mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye miradi ya uzalishaji kuna mwenzetu mmoja alichangia kwamba…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Naibu Waziri hapo ndiyo ambapo kidogo huwa tunachanganyikiwa, mwaka ujao kwa maana ya 2023 au mwaka 2024 maana unasema mnatarajia ikamilike mwaka ujao, wakati taarifa tulizonazo ni 2024.

NAIBU WAZIRI WA NSHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi wa kutoa umeme Mwalimu Nyerere kuuleta Chalinze unakamilika mwaka wa fedha huu. Nina maana ya Januari kuelekea Juni, mwaka wa fedha huu. Kwa hiyo, kwa program tuliyokuwa nayo itakamilika kabla ya Bwawa la Mwalimu Nyerere kukamlika ambalo kwa mujibu wa mkataba wa extension nitakaousema baadae inatakuwa kuwa Oktoba mwakani. Kwa hiyo, ni mwaka wa fedha huu tuliopo sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi ambayo mpango umeitaja kwa ajili ya uzalishaji. Tunao Mwalimu Nyerere, megawatt 2115, tunayo Rusumo unakamilika muda siyo mrefu megawatt 80, tunayo Ruhuji inakuja megawatt 358, tunayo Rumakali megawatt 222, tunayo Kikonge megawatt 300 tuna miradi ya upepo na jua megawatt 300, tunayo Kinyerezi One Extension megawatt 185, zote hizo tunatarajia kwamba zitatupatia umeme kwa mujibu inavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba unipe nafasi kidogo ya kueleza mambo mawili kwenye mradi wa Mwalimu Nyerere.

MWENYEKITI: Sasa kila Waziri anaomba apewe nafasi kidogo tu sijui nimkate mmoja ili ndiyo niwe nimezigawanya hizo? Haya dakika moja malizia.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa sababu ya muda nizungumzie vitu viwili tu. Kimoja muda tuliouongeza kwenye Bwawa la Mwalimu Nyerere ni mwaka kwa mujibu wa mkataba, tumeongeza mwaka mmoja na muda huo utakapoisha ndiyo tutaanza kugombana kuhusu nani kachelewesha mradi.

MWENYEKITI: Mwaka mmoja ndiyo mpaka lini?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni Oktoba mwakani kwa mujibu wa mkataba tuliosaini. Iko taarifa na mpango kazi wake aliouleta anapoomba miaka miwili sisi tulimwambia tunampa mwaka mmoja na wenzetu wataalam wanaendelea kuchanganua ule mpangokazi wa utekelezaji ili u-fit mwaka mmoja lakini mkataba wa nyongeza extension of time ni mwaka mmoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kidogo kuhusu hii habari inayosemwa ya liquidated damages, taarifa sahihi ni kwamba liquidated damage kwenye mkataba wa Mwalimu Nyerere ni 0.1% kwa kila siku kwa maximum ya asilimia Tano siyo asilimia Kumi siyo zaidi ya hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni kwenye CSR tunaambiwa tunatoa taarifa kwamba tungezikata hizi pesa. Mkataba unatueleza kwamba tumpe Mkandarasi atekeleze CSR, tulikuwa hatujakubaliana miradi ya kutekeleza sasa tumekubaliana Mkandarasi ataanza kutekeleza CSR za bilioni 263 na tuko ndani ya muda na tutakamilisha kazi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata nafasi hii na mimi nianze kwa kuunga mkono hoja bajeti ya Wizara ya Nishati na nikiwaomba Waheshimiwa Wabunge wote muipitishe, na ni kwa sababu hizi chache kwa muda niliopata nitakazozisema.

Mheshimiwa Spika, namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, namshukuru Mheshimiwa Makamu wa Rais pamoja na Waziri Mkuu, na hasa kimahsusi Mheshimiwa Rais kwa kuniruhusu sasa ninasoma Bajeti ya Wizara ya Nishati au ninahudhuria au inasomwa nikiwepo kwenye Wizara hii kwa mara ya tatu; ninamshukuru sana kwa kuendelea kuniamini. Na mimi ni moja wapo kati ya wale wachache ambao wanaweza wakaeleza jitihada na mwelekeo mzuri wa Wizara hii kwa kuwahudumia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana wewe na ninakupongeza kwa jitihada zako na uongozi wako mzuri nakutakia kheri katika lile ambalo wenzangu wote wamelisema. Nawashukuru sana Waheshimiwa Mawaziri wenzangu, Waheshimiwa Wabunge lakini kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Waziri, January Makamba kwa malezi yake kwangu mimi kama mdogo wake lakini kwa kutuongoza vyema Wizarani mimi pamoja na wenzangu ambao tunamsaidia kazi nawapongeza pia. Mwisho lakini si kwa umuhimu, nawashukuru waajiri wangu wa Jimbo la Bukoba Mjini kwa kuendelea kuniamini na kunipa ushirikiano nikiendelea kutekeleza majukumu ya kitaifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara imepokea shukurani na pongezi nyingi sana. Hapa mwanzo kabisa nieleze, shukurani hizi na pongezi hizi ni za Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. Sisi ni wawakilishi, ni wajumbe na ni watenda kazi wake kwa niaba ya Watanzania; na tutaendelea kufanya kazi hii kwa sababu tunaipenda na tunaiweza na tuko tayari kuendelea kulitumikia Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, lakini kama raia na wananchi wa kawaida tu na mimi naomba nitoe shukurani zangu kwa Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuamua kwa mara ya kwanza kuruhusu fedha itengwe kwa ajili ya kupeleka Gridi ya Taifa kwa Mkoa wa Kagera kwa kujenga line ya kutoka Benako kwenda Kyaka. Kwa hiyo na sisi watu wa Kagera tunafurahia matunda mazuri na wito wake mzuri kwa kuwahudumia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijielekeze kwenye hoja mbili ambazo nitamsaidia Mheshimiwa Waziri kujibu na kwa muda nitakaokuwa nao naamini nitafanikiwa. Maeneo hayo ni gharama za kuunganisha umeme lakini pia nitaenda kwenye gharama za umeme vijijini au umeme vijijini kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge takribani wote wamezungumzia kuhusiana na gharama za kuunganisha umeme. Tumewasikia na tunawaelewa na tunatamani jambo hilo litokee kwa sasa, lakini si rahisi na hatuwezi kulifanya kwa haraka sana namna hiyo. Sababu ni kwamba tunahitaji fedha zaidi.

Mheshimiwa Spika, gharama za kuunganisha umeme halisi ni wastani wa shilingi 700,000 kwa wale ambao wapo ndani ya mita 30. Kwa hiyo, pale ambapo tunaunganisha umeme kwa shilingi 320,000 kwa mjini maana yake Serikali ya Awamu ya Sita imeweka ruzuku ya takribani shilingi 380,000 ili iweze kuunganisha umeme. Kwa wenzetu wa vijijini ambao wanaunganisha kwa 27,000 imewekwa takribani ruzuku ya shilingi 670,000 ili waweze kuunganisha umeme.

Mheshimiwa Spika, gharama za sasa zina ruzuku kubwa ya namna hiyo. Sasa, ruzuku maana yake ni fedha ambayo inalipwa na mwingine ili mwingine apate huduma. Kwa hiyo, it’s either ilipwe na mwananchi au ilipwe na TANESCO au ilipwe na Serikali. Tulivyofanya hesabu baada ya mabadiliko ya kurudi kwenye bei ambazo tulikuwa tukizitumia zamani Januari mwaka jana, TANESCO ilibaini ongezeko la shilingi bilioni sita katika makusanyo ya gharama za kuunganisha. Kwa maana hiyo kwa mwezi TANESCO inahitaji bilioni sita ili kuunganisha watu kwa gharama ya shilingi 27,000 kwa mjini na inahitaji takribani bilioni kama saba kuunganishwa wale wa vijijini. Kwa maana nyingine tukitaka kuunganisha Watanzania wote wanaohitaji umeme tunahitaji takribani bilioni 13 ya ruzuku ili kuweza kuunganisha kwa shilingi 27,000.

Mheshimiwa Spika, ukiipiga hii kwa mwaka ni takribani bilioni 156. Sasa jambo hili tunalielewa na tunatamani litokee lakini sasa bilioni 156 inatoka wapi? Tunawaombeni sana Waheshimiwa Wabunge mturuhusu tuendeelee kuchakata tuone namna ya kujibana hapa na pale ili fedha hii ya ruzuku ipatikane, gharama hizi ziweze kupunguzwa kwa wananchi ili tuweze kupata huduma hiyo vizuri kabisa.

Mheshimiwa Spika, ni dhahiri kabisa Mheshimiwa Rais anayonia, na pale ambapo tumekuwa tukikabwa sana amefanya. Alitoa bilioni 100 kuweka ruzuku kwenye mafuta na amekuwa akitoa ruzuku kwenye mbolea na kwenye maeneo mengine. Tunaamini kwa kujibana na kwa kuweka viapumbele mbele hili nalo utalifanikisha. Kwa sasa shughuli ya kubaini maeneo ni yapi kwa uwezo wa wananchi kwa uwezo wa kiuchumi linaendelea, na litakapokamilika tutakuja kuliunganisha pamoja na hili ili sasa tuweze kufikia sehemu ambapo tutaunganisha wananchi wetu kwa gharama nafuu. Ni jambo zuri lenye kuleta kheri lakini linahitaji mjadala mkubwa Serikalini kuweza kubaini sehemu ya kupata fedha hiyo, na mimi naamini kwamba tutalifanikisha.

Mheshimiwa Spika, niende kwenye jambo la pili la umeme vijijini. Waheshimiwa Wabunge takribani wote waliposimama wamelizungumzia jambo hili, na ni jambo la muhimu kweli na katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya uchaguzi imeelekeza ifikapo 2025 vijiji vyote viwe vina umeme. Sisi hatuna wasiwasi hata kidogo, wala 2025 hatutafika jukumu hili na sharti hili la ilani litakuwa limekamilika. Mwaka huu tutahakikisha kwamba vijiji vyote vinapata umeme. Kwa sasa overall tumefikia asilimia 72 ya Mradi wa REA III Round II. Yapo maeneo ambapo tumefanya vizuri sana. Lot namba 30 ya Simiyu yenye Wilaya ya Maswa na Meatu tumemaliza asilimia 100. Lot namba 18 ya Morogoro vijijini asilimia 100, lot namba 23 ya Pwani wilaya zote asilimia 100. Lot namba 38 ya Tanga, Wilaya ya Kilindi, asilimia 100, lot namba 14 ya Mkoa wa Mara, na wamesema hapa, asilimia 100. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunakiri kwamba bado kuna sehemu hatujafanya vizuri. Na mpaka sasa baada ya jitihada zilizoanza Januari mwaka huu tumebakiza Lot nne ambazo tunaona hatukaa sawa. Lot namba moja, lot namba 27, lot namba 39 na lot namba 25. Waheshimiwa Wabunge humu wamesema, tunaomba mtuamini, tumeweka mikakati, tuemeweka jitihada na tunakimbizana na wakandarasi hawa, tutafanikisha. Lakini si maneno tu, Waheshimiwa humu wengine wamesema tufungue LC, LC tayari zimefunguliwa na wale ambao wanakidhi vigezo watachukua pesa ili waweze kupata vifaa kwa wakati mahsusi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeongeza wasimamizi. Waheshimiwa Wabunge wote mnafahamu vijana wameripoti kwenye majimbo yetu kwa ajili ya kuendelea kutoa taarifa za siku hadi siku ili mradi uweze kusimamiwa vizuri. Tumeongeza wahandisi wa REA kwenye level za mikoa, tumeongeza speed kwenye taratibu za malipo, maana malipo yanakwenda REA, yanakwenda TANESCO na yanakwenda Wizara ya Fedha; yalikuwa yanachukua muda. Tume-develop mechanism ambayo itatufikisha kwa haraka mwishoni.

Mheshimiwa Spika, lakini hatujaishia hapo tu, tumeweka mechanism mpya ya miradi mipya inayokuja ili tusiingie kwenye matatizo ambayo tumekutana nayo. Moja wapo ya sharti ni kwamba kama hujafikia asilimia fulani za mradi mwingine hauto qualify kupata mradi mpya, na hii tayari tumeanza kuitekeleza; na katika hili hatutazamani usoni, tunahakikisha kwamba tunalisimamia vyema.

Mheshimiwa Spika, kuna mkandarasi ambaye alitajwa hadharani si vyema tukaliacha hivi hivi. Mkandarasi anayefanya kazi ya Tanga kwenye maeneo kadhaa lakini ana kazi pia Mkoa wa Kahama. Mkandarasi huyu hakufanya vizuri Tanga, anaitwa Tontan. Kwa upande wa Kahama Mheshimiwa Iddi na Mheshimiwa Cherehani wametoa Ushahidi; anajitahidi sana kufanya kazi nzuri kwenye eneo la Kahama.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kwa Korogwe tuna shughulika naye na hatua zimeshaanza kuchukuliwa liquidated damage tumeshaanza kukata. Kwa hiyo, tunaichukua Lot ya Korogwe kama ameshindwa kufanya kazi tunashughulika naye huko. Lot ya Kahama ambayo anafanya kazi vizuri kwa kujitahidi tunaendelea kumtazama kwa karibu. Lakini ilisemwa kwamba amepata kazi nyingine TANESCO; ni kweli amepata kazi ya kujenga line ya kutoka Ubungo kwenda Ununio, na alipata kazi kabla hatujajua haya mengine. Alikuwa ameonekana atapata kazi nyingine mbili lakini zimesitishwa kwa sababu alionekana atatusumbua. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini aliwahi kufanya kazi nyingine, aliwahi kujenga line ya Dege kuja mpaka Kurasini, aliifanya vizuri. Kwa hiyo, matatizo aliyoyapata sisi hatuyatazami kama ni matatizo ya jumla, tunatazama kwenye mradi husika. Kwenye mradi wa Korogwe tutashughulika naye kisawasawa mpaka tupate haki yetu na yeye apate haki yake. Huko kwingine tutaendelea kuhakikisha kazi inafanyika vizuri. Hii Lot ya kutoka ubungo kwenda Ununio ameshaleta bank guarantee. Akianza kusuasua tunakula kichwa kwa sababu kazi yetu ni kuhakikisha kwamba huduma inawafaikia wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi niombe mtupe nafasi tena tuendelee kusimamiana na hawa wenzetu. Umeme vijijini ni siasa kwa kila mtu lakini ni huduma kwa wananchi, na tutahakikisha tunaweza kulifanya hili vizuri. Lakini pia pale ambapo mkandarasi amesua sua leo tusifute na record zake za jana na juzi, huenda ikawa watumishi labda walikuwa wamepitia njia ambazo si sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, alisema mkandarasi aliyefilisika kwenye Kinyerezi I Extension, mkandarasi huyo huyo alitujengea Mradi wa Kinyerezi I vizuri kabisa na ukakamilika, unafanya kazi mpaka leo. Mkandarasi huyo huyo alitujengea mradi wa Kinyerezi II vizuri kabisa umekamilika mpaka leo unafanya kazi kwa zaidi ya dola milioni 300. Alipoingia kwenye Kinyerezi I Extension yaliyomkuta yalimkuta akapata shida. Isionekana tulikuwa na mkandarasi wa hovyo na ambaye hafai alifanya kazi nyingine lakini huko tupaache Kinyerezi I Extension imekamilika na Mega Watt 135 zimeshaingia mradi unafanya kazi vizuri na umeziba ma-gap ambayo tulikuwa tuna matatizo katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu ya muda, eneo la umeme wa vitongojini nitamuachia Mheshimiwa Waziri aje aliseme kwa upana wake kwa sababu lina kishindo kikubwa. Kwenye Hotuba ya Mheshimiwa Waziri tulisema nia ya kuendeleza Wizara ni kuifanya sekta ya nishati kushamirisha shughuli za biashara, uzalishaji na maendeleo ya sekta nyingine zote za kijamii na kiuchumi, ndivyo tunavyoiona Wizara ya Nishati. Na jukumu hilo kama nilivyotangulia kusema kazi hii sisi tunaipenda na tunaiweza. Tunaomba muendelee kutuamini na mtupe nafasi ya kufanya hii kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwaombe Waheshimiwa Wabunge, waipitishe bajeti hii ambayo kama ilivyosemwa na wenzangu ina component kubwa ya miradi, ina component ndogo sana ya OC na kwa ajili ya mambo mengine. Tukishafanikiwa hili tunaamini baada ya bajeti kupitishwa shughuli itaanza kwa kasi. Ari na moyo tunao na tunaweza kufanya kazi hii kama mnavyotuona na jinsi mlivyotupongeza na kutupa hamasa na shukurani ambazo nimesema zote zielekezwe kwenye mwenye nazo, Mheshimiwa Rais. Tunawashukuru sana, na kwa nyuso navyoziona naamini shughuli ilishakamilika na namuomba Mwenyezi Mungu aibariki iwe hivyo hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuyasema hayo ninaomba kuunga mkono hoja na Mwenyezi Mungu awabariki wote, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nashukuru kwakupata nafasi ya angalau kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri wa Nishati nikiwa ni msaidizi wake, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutubariki na kutupa nafasi ya kukutana tena na kuleta zawadi nyingine ya Mama kama ambavyo amekuwa akisema Mheshimiwa Mwijage kutoka katika Wizara ya Nishati kama ambavyo imeanza kutolewa tangu jana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa sababu ya muda nitakimbia kimbia ili nimuachie Mheshimiwa Waziri nafasi pana zaidi ya kuweza kueleza mambo makubwa zaidi ya kisera ambayo yamechangiwa na Waheshimiwa Wabunge katika nyanja mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda pia kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Moja, kwa kuendelea kuwa na imani na mimi na kunibakiza nitumie neno hil,o katika Wizara hii ya Nishati nikiendelea kumsaidia Mheshimiwa Waziri majukumu lakini na kumsaidia yeye pia, lakini cha muhimu zaidi mimi nimshukuru kwa sababu yeye ndiyo anayefanya kila kitu katika Wizara yetu ya Nishati nasi tunaleta ujumbe ambao anatupatia yeye. Haya mambo yote ambayo mmeyasema hapa sisi tunayofaraja kwamba Mheshimiwa Rais ametuamini na kuturuhusu tuje kuyasema kwenu na kupokea maoni yenu na tunawahakikishieni kwamba hatutawaangusha ninyi wala hatutamuangusha Mheshimiwa Rais katika utekelezaji wa yale yote ambayo tumekubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ajili ya muda mimi niseme maeneo kama matano lakini kwa haraka haraka. Kwanza yametolewa maoni na maswali mengi ya msingi kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge katika maeneo mbalimbali, kwa niaba ya Serikali niseme mambo kadhaa ambayo yamesemwa yapo wazi kabisa na tunayachukua tunayafanyia kazi mengine yanahitaji mjadala mpana zaidi, tutauleta hapa ili uweze kufanyiwa kazi lakini kwa sababu ya muda sasa angalau nitaje machache ambayo moja kwa moja Serikali imeyachukua na tunaahidi kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo la mafuta kwa haraka haraka nikuboresha miundombinu ya kupokea mafuta pale Bandari ya Dar es Salaam na bandari nyingine na kama tulivyosema na ambavyo mmesema nyie zipo gharama ambazo zinaongezeka katika bei zetu za mafuta kwasababu ya miundombinu yetu ya kupokea mafuta kutokuwa mizuri limesemwa na Waheshimiwa Wabunge wengi na tunalichukua na litaanza kufanyiwa kazi mara moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kujenga single receiving terminal, Mheshimiwa Waziri mara kadhaa ameeleza jitihada ambazo Wizara inazifanya jinsi ambavyo tumewatafuta wadau mbalimbali ili hilo jambo liweze kufanyika na itatusaidia sisi kuwa na nafasi nzuri zaidi ya kuweza kufanya biashara ya mafuta katika hali ambayo inatuwezesha kuwa na ushindani mzuri. Wameshauri kwamba katika muda huu ambao tunajiandaa sasa tunakamilisha taratibu za kujenga single receiving terminal basi matenki yetu ambayo yapo pale tipper ambayo sisi tunayamiliki kwa sehemu kubwa basi yaweze kutumika kufanya kazi hiyo. Niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba hilo nalo limechukuliwa na tayari Serikali imeshaanza kulifanyia kazi na katika muda mfupi ujao mafuta yataanza kushushwa pale tipper.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wameshauri pia TBS iache kuwa inazunguka na sampuli za mafuta kutoka maeneo mbalimbali na kwenda kwenye maabara moja zitengenezwe maabara kila eneo ambapo mafuta yanashushwa na hilo limechukuliwa na katika muda mfupi litafanyiwa kazi na wanaotoka maeneo hayo ni mashahidi watakuja kuwaambieni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia Waheshimiwa Wabunge wameshauri zitengenezwe kanuni za kuwezesha biashara ya mafuta katika vijiji vyetu kuwa rafiki zaidi. Niseme kwanza mwaka 2020 zilishatengenezwa kanuni za kuweka mazingira rafiki katika maeneo ya miji na vijiji kufanya biashara za mafuta lakini hiyo kama haitoshi Serikali tayari imeanza kupitia upya kanuni hizo ili kuona namna ambavyo inaweza ikashusha zaidi zile gharama za wale watu wanaweka katika vituo maeneo ya vijijini na katika muda mfupi tutaona matokeo yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati pamoja na Waheshimiwa Wabunge wameshauri kwamba mfumo wetu wa BPS au mfumo mwingine wowote utakaotumika katika kuagiza mafuta uzingatie kuhakikisha kwamba mafuta yanayokuja ni safi ni salama na uhakika wa kupatikana kwa mafuta hayo. Nasi tunawahakikishieni Waheshimiwa Wabunge kwamba wakati wote ambapo tunatafuta njia nzuri zaidi ya pamoja ya kuwezesha gharama za mafuta kushuka lakini tunahakikisha tunazingatia uhakika wa upatikanaji wa mafuta katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri mwingine uliotolewa ni kuweka mazingira mazuri ya kuhakikisha wale wanaoleta mafuta wanaochezea chezea taratibu zetu hizi wakaleta katika compartment yao unakuta mtu ana Meli na compartment tatu, compartment moja ina mafuta machafu nyingine mbili zinakubalika tuwashughulikie sawasawa ili kuepusha kutuchezea chezea na kututania mara kwa mara. Nami kwa niaba ya Serikali niwaahidi tutaendelea kushughulika nao kwelikweli ili waendelee kupata adabu na kutotuchezea chezea kwa sababu sisi ni hub ya wengine wanaotutazama kutoka huko nyuma yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tumeshauriwa kuhakikisha kwamba tunafanyia kazi chanzo cha umeme cha cha jotoardhi (geotherm) kwa kuhakikisha kwamba sheria ile tunairekebisha ili iweze sasa kukidhi matakwa ya kuwa chini ya Wizara ya Nishati na kuiwezesha pia Wizara yenyewe kuwa ndiyo msimamizi sasa mkubwa wa TPDC na kuipa kipaumbele TPDC kwa ajili ya kuweza kuleta mabadiliko katika eneo la nishati ya joto ardhi kama wenzetu Wakenya walivyofanya. Tuwahakikishieni kwamba hilo tumelichukua na kwenye bajeti hii pesa imetengwa zaidi ya Bilioni Ishirini kwa kuendelea kuiwezesha TPDC kufanya kazi zake katika maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ni maeneo ambayo kwa uchache kabisa yapo mengi sana nimeona niyagusie na mengine Mheshimiwa Waziri atakuja kuyamalizia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa ufupi niende kwenye maeneo mengine mawili. Eneo ambalo kila Mheshimiwa kila aliposimama ameligusia eneo la umeme vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunafurahi kwanza kwa Mheshimiwa Rais kuendelea kui-support sekta ya nishati kwa kupeleka umeme vijijini bila kupepesa macho bila kupepesa kope, katika hili Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amepambana kwelikweli. Ni uwazi usiopingika kwamba kwa sehemu kubwa sana umeme vijijini siyo biashara umeme vijijini ni huduma kwa sehemu kubwa sana. Kwa sababu umeme ule unaounganishwa tunazifahamu familia zetu za vijijini, kwa sehemu kubwa mtu anaweka umeme wa Shilingi 9,150 unit 75 anakaa nazo miezi mitatu, miezi sita siyo biashara. Pamoja na hilo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ameelekeza pelekeni umeme kwenye vijiji, pelekeni umeme kwenye vitongoji na gharama ibakie kuwa Shilingi 27,000. Katika hili Wizara ya Nishati tunampongeza sana Mheshimiwa Rais, Trilioni Moja na Bilioni Mia Mbili na Hamsini zipo zinaendelea kupelekwa katika maeneo yetu kwa ajili ya kuhakikisha kwamba miradi ya REA inakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwenye eneo jingine tulisaini mikataba mingi kwa ajili ya kupeleka umeme vijijini, mikataba ile mingi ilikuwa inadondokea Desemba mwaka 2022, mingine ilikuwa ina overlap Desemba, 22 kwa sababu mkataba unamiezi 18. Sasa tuwahakikishieni kwamba wale ambao walitakiwa kukamilisha mikataba mwezi Desemba ambao walianza mapema, tutapambana nao na kuhakikisha kwamba kipindi hicho kikifika mikataba inakamilika. Wale ambao mikataba yao ilikuwa ina-overlap basi tutakubali kuhakikisha kwamba muda ule wa mkataba unafikiwa lakini endapo kutatokea kuongezeka kwa muda wa kukamilisha mkataba yapo mambo kadhaa ambayo yatasababisha kuongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo yapo mawili chanya na mengine ni hasi, jambo la kwanza sisi wenyewe Waheshimiwa Wabunge tunapenda maeneo tunayopeleka umeme yaongezeke, sasa unapoongeza scope ya kazi siyo rahisi kumbana mtu afanye kazi katika muda uleule mliokuwa mmekubaliana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo jingine ni kuongeza wigo sasa si kazi ya awali lakini Mheshimiwa Waziri tayari ameshatoa ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kuongeza kilometa mbili kwenye maeneo yetu ya vijiji sasa inapoongezwa kilometa mbili si rahisi sasa ukamilishe ndani ya uleule muda uliokuwepo wa awali. Changamoto hasi ambazo tumezipata cha kwanza ni kupanda kwa gharama za vifaa, ni uwazi usiopingika gharama zimepanda lakini tunahakikisha kwamba jambo hili tunalifanyia kazi lakini pia tumebadilisha kutoka kwenye goods kuja kwenye works. Nisema kidogo hapa huko nyuma tulikuwa tunafanya mikataba ya upelekaji wa umeme vijijini kwa kutumia taratibu zinazoitwa goods ambapo mnampa Mkandarasi fedha ya kununua vifaa vyote asilimia karibia 80 ya mkataba ananunua vifaa anavitunza halafu ile asilimia 20 anaanza kufanyia kazi. Tuliona mtu anaponunua vifaa akapata faida yake anaingia mitini, sasa tukabadilisha utaratibu twende na works kwamba tutakulipa fedha kidogo advance payment asilimia 20 utanunua vifaa kidogo na pesa ya mobilization halafu sasa ukifanyakazi tukaja tukakagua tunakulipa. Sasa kwenye hiyo habari yakuja kukukagua tukakulipa ili ukanunue vifaa vingine tumekutana na habari ya kupanda kwa bei lakini tunahakikisha kwamba tunashughulika nalo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya nini katika eneo hili, hatua za utekelezaji tumeshazisema mara kadhaa, jambo la kwanza ambalo tumelifanya. Tumewaleta Wakandarasi wote chini ya usimamizi wa Mheshimiwa Waziri January Makamba hapa Bungeni, wamekaa hapa siku tatu, Waheshimiwa Wabunge wameenda wamewaona, wamewahoji wamejua shida iko wapi na tunatatua vipi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo tumelifanya ni kuongeza usimamizi. Mheshimiwa Waziri ameshasema, tunao wasimamizi ngazi ya Kanda, tunao wasimamizi ngazi za Mikoa lakini sasa wanakuja wasimamizi ngazi za Jimbo, waje wasimamizi wa miradi yetu ya REA kwenye Majimbo yetu. Ukiamka unaamka naye ukilala unalala naye na hiyo ni zawadi nyingine ya Mama ambayo Mheshimiwa Waziri ametuambia, nia ni kuhakikisha kwamba tunafikia sehemu ambapo mradi hautakwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu na la mwisho katika eneo hili; tumekaa na wakandarasi, tumejadiliana nao, tumekubaliana kwamba jambo hili sasa liishe, waendelee na kazi wakati sisi tunaendelea na mchakato wa kurekebisha mikataba yao na kuwawekea katika mazingira mazuri. Tunaahidi kwamba mikataba hii itakamilika, tutaisimamia vizuri kabisa na itakuwa ni ya tija kwa Watanzania wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika vitongoji tayari zawadi nyingine ya Mama imeshasemwa, tuko katika taratibu za kutafuta shilingi trilioni 6.5 kwa ajili ya kuhakikisha vitongoji vile vyote zaidi ya 30,000 vinapelekewa umeme kwa pamoja katika muda mfupi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda niende kwenye eneo lingine la mwisho la TANESCO; kila Mbunge aliyesimama amezungumzia kukatika kwa umeme. Wanasema mnyonge mnyongeni, lakini haki yake mpeni. Katika eneo hili hali siyo mbaya kama ilivyokuwa siku chache zilizopita, tulisimama Bungeni, tukakiri tatizo na upungufu lakini tukawaambieni njia za kuchukua na mimi nilikuwa mmojawapo niliyeahidi kwamba TANESCO hatuajiri mtu kwa ajili ya kukatakata umeme na kweli inaonekana wazi kwamba umeme haukatwi bila sababu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini umeme unakatika? Iko miundombinu ambayo ni chakavu inatuletea shida; kuna mambo ya asili yanatokea, radi, mvua, tingatinga na mambo kama hayo; kuna miundombinu kuzidiwa na umeme, transfoma tuliifunga, tulikuwa tuna watu 25 watu wameongezeka wamekuwa 50/70 hatujaibadilisha, tunakuwa na tatizo. Tumefanya nini katika eneo hili? Mheshimiwa Rais ametupa zawadi nyingine ya shilingi bilioni 500 ambayo itakuja kumaliza changamoto zote hizi katika maeneo yetu, zitapelekwa kujenga vituo vya kupoza umeme, zitapelekwa kujenga njia za kupeleka umeme, zitapelekwa kubadilisha transfoma na kuwekwa kubwa, zitapelekwa kutengeneza miundombinu mipya, tunakoelekea habari ya kukatikakatika kwa umeme itakuwa ni historia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachomshukuru Mwenyezi Mungu wakati mabadiliko haya mazuri yanakuja na zawadi za Mama zinakuja, niko hapa tayari kutumika kuendelea kuhakikisha kwamba watanzania wanapata kile walichokistahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu ya muda ninaomba niishie hapo, nashukuru sana ushirikiano ambao Waheshimiwa Wabunge wanatupatia na mimi binafsi niwaahidi nitaendelea kutumika na baada ya Bunge hili mtatuona sana majimboni tukiwa tunahakikisha tunafuatilia yale tuliyoyaahidi na kuyafanyia kazi kwa niaba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa nafasi hii. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kwanza kuunga mkono hoja ili lolote likitokea huko mbele basi niwe kwenye safe side. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa muda huu mfupi ili na mimi niweze kusema kidogo tu wakati huo nikimuachia Mheshimiwa Waziri nafasi ya kueleza na kuweka commitment za Serikali kwenye maeneo ambayo Waheshimiwa Wabunge wamechangia.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa shukrani, nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa uhai, afya na nimshukuru Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan kwa kuniona mimi kijana na akaamua kunipa majukumu haya makubwa. Nimhakikishie tu kwamba kwa niaba ya vijana wenzangu ambao tunaendelea kutumika katika nafasi hizi hatutamuangusha yeye wala Watanzania katika utekelezaji wa majukumu yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niwashukuru viongozi wa Kitaifa, Mheshimiwa Makamu wa Rais na Waziri Mkuu. Kipekee kabisa nikushukuru wewe kwa jinsi unavyotuongoza na kutujenga sisi Wabunge na hasa sisi Wabunge vijana na Waheshimiwa Wabunge wote ambao wapo humu kwa ushirikiano mkubwa ambao wanatupatia kama Wabunge, lakini mimi kwa nafasi yangu kama kiongozi kwenye nafasi ya Uwaziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Mheshimiwa Waziri wa Wizara yetu ya Nishati kwa kuendelea kuwa kiongozi, jemedari shupavu na aliyekakamaa kabisa na kutufikisha hapa ambapo wengi tunaogopa tunadhani hatutafika, lakini kwa maelekezo ya wakubwa wetu na yeye Wizara yetu imeendelea kufanya kazi ambazo Watanzania wanazitegemea. Pia niwashukuru watendaji wengine wote wa Wizara yetu ambao kwa kweli mengi tunayoyasema na kuyafanya hapa ni yale ambayo wao wametushauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mnyimi wa fadhila nisipowashukuru wananchi wa Jimbo la Bukoba Mjini walioamua kukichagua Chama cha Mapinduzi kwa kunipa mimi kura za kutosha na kunituma kijana wao kuja kutumikia Taifa katika maeneo haya. Nimshukuru pia mke wangu kwa kuendelea kunivumilia na kunipa nafasi ya kufanya majukumu haya, lakini na familia kwa ujumla na maisha yanaendelea vema. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitazungumzia maeneo matatu tu, kwa haraka haraka, maeneo mawili ni ya ufafanuzi mdogo na Mheshimiwa Waziri atakuja kumalizia. Eneo la kwanza Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamezungumzia kuhusu kukatika kwa umeme. Sababu za kukatika kwa umeme zitaelezwa, lakini mimi niseme tumejipanga kupitia bajeti tunayoomba mbele yenu lakini tumejipanga kufanya yafuatayo kwa uchache wake ili kuhakikisha basi umeme unakuwa haukatiki mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, cha kwanza tutarekebisha miundombinu kama ambavyo tumekuwa tukifanya, tutaendelea kupanua wigo wa kurekebisha miundombinu. Pia tutasogeza vituo vya kupoza umeme karibia na watumiaji ili kupunguza ule wigo wa umeme kupotea na vimetajwa kwenye bajeti yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tutafunga vifaa mbalimbali vya kitaalam vya kuhimili vitishio vya kiasili kama radi, mvua na vitu kama hivyo nitavitaja baadaye kitaalam. Pia tunaweka njia ile ya kupitisha umeme salama kwa kuendelea kufyekea yale maeneo ili yasipate madhara ya miti kuangukia nguzo na nyaya za umeme.

Mheshimiwa Spika, la mwisho siyo kwa umuhimu kuendelea kuwasimamia watumishi tunaofanya nao kazi na hasa wale wachache ambao ni wazembe, wanaosababisha upotevu wa umeme na kuonekana kwamba umeme unakatika pengine bila sababu za msingi. Hivi juzi mmeona hatua ambazo Mheshimiwa Waziri Mkuu alizichukua pamoja na Mheshimiwa Waziri wetu katika kuhakikisha kwamba watumishi wanakuwa waadilifu na wanatumika vizuri kwa ajili ya kuwaletea maendeleo Watanzania.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ambalo nataka nizungumzie kidogo tu ni kuhusu miradi ya REA. Kwa nini miradi ya REA mingine imekuwa ikichelewa kukamilika? Sababu zipo nyingi lakini mimi nitaje kidogo tu, mojawapo ni ile kuongezeka kwa wigo wa kazi ambayo mkandarasi amekuwa amepewa mara ya kwanza. Alipewa vijiji sita lakini tumefika site tumekuta vijiji vinavyohitaji umeme zaidi ni kama tisa au kumi kwa vyovyote vile ule muda wa awali tunajikuta tunatakiwa kuongeza ili kukamilisha yale ambayo yanatakiwa kufanyika.

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili ambalo ni la kuelezeka ni pale ambapo baadhi ya maeneo yanakuwa hayafikiki labda ni kwenye mapori, hifadhi au hali ya hewa ya mvua basi hapapitiki kwa sababu ya miundombinu kuchukuliwa na maji tunajikuta tunachelewa katika maeneo hayo. La tatu ambalo pia linatokea ni mkandarasi kujikuta ana kazi nyingi na mwisho wa siku ikawa ni ngumu kuzimaliza kwa wakati aliopewa kwa sababu pengine ya usimamizi kuwa mgumu kidogo na hilo pia tutalizungumza kwamba tumechukua hatua.

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kama alivyosema mwenzangu mmoja lakini kama alivyowahi kusema kiongozi wetu mstaafu wa Mkoa wa Kagera Mama yetu Prof. Tibaijuka kwamba kadri unavyopanua zaidi ndivyo watu wanavyokuwa na hamu zaidi. Sasa Serikali ya Awamu ya Tano na ya Sita zimeendelea kupanua wigo wa kupata umeme. Katika kupanua wigo wa kupata umeme wananchi wamekuwa wakiuhitaji sana na matumizi yamekuwa ni makubwa na hiyo sasa inapelekea pengine umeme usionekane wa kutosha lakini jitihada za Serikali ni wazi kabisa mambo yataendelea kuwa mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ambalo naomba nilizungumzie, mimi kwa nafasi yangu ya Unaibu Waziri na kwa jinsi tunavyofanya kazi katika michango mbalimbali iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge nimeona tunayo mambo kama 15 ambayo tunatakiwa kujivunia lakini pia yatakuwa ni chachu ya sisi kuendelea kufanya kazi usiku na mchana kuhakikisha Watanzania wanapata nishati ya umeme katika maeneo yaliyopo na umeme wa uhakika, sahihi, kila wakati na kwa gharama nafuu. Mambo hayo nikiyataja kwa haraka haraka tu, naamini dakika zilizobaki zitanitosha kuyajata hayo mambo 15; la kwanza ni bajeti ya Wizara ya Nishati kuwa na fedha ya maendeleo asilimia 98.9, hii fedha nyingine ni asilimia moja tu. Kwa hiyo, Wizara ya Nishati tumejipanga mkitupitishia kama ambavyo nitaomba mwishoni kufanya kazi kwa fedha tuliyopewa asilimia 98, tunaamini tutafika mbali kabisa.

Mheshimiwa Spika, lakini tumejipanga kuendelea kusimamia bora rasilimaliwatu na rasilimali fedha kama ambavyo imekuwa ikifanyika. Pia tunahakikisha kwamba tunafikisha ile adhma ya kuwa na umeme unaotosha kwa Watanzania wote. Kwa sasa tunao uwezo wa kuzalisha megawatt karibu 1,602, lakini jana usiku ndio tumekuwa na matumizi ya juu megawatt 1,201, kwa hiyo bado tuna kama megawatt 400. Sasa miundombinu ya kuzifikisha hizo zote kwa Watanzania ndiyo ambayo tunaomba sasa mtusaidie ili tuweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoomba kwamba naomba…

SPIKA: Bado dakika tano.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, eneo la nne ni kuendelea kuzalisha umeme katika miradi mbalimbali mkubwa sana ukiwa wa Mwalimu Nyerere, lakini pia tunayo Rusumo, tumesaini mkataba mwingine wa Malagarasi na tunaamini kwamba tutakuwa katika nafasi nzuri na miradi mingine. Pia tunahakikisha tutapeleka umeme katika vijiji vyote vilivyobakia takribani kama 1,500 kabla ya mwezi Disemba 2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tutaendelea kuboresha miundombinu yetu ya umeme kwa kufunga vifaa mbalimbali nilivyokuwa navisema, tunafunga surge arrester, combi unit, auto recloser socket breaker, AVR wameitaja hapa asubuhi na vitu vingine kama lightning arrester, tunahakikisha kwamba sasa umeme ukishakuwepo unaweza kuhimili hayo mambo ambayo ni ya kina naturally yanayoweza kuja kuzuia umeme wetu usiwe wa uhakika.

Pia tumejitahidi kutoa kazi nyingi kwa wakandarasi kidogo kidogo ili mkandarasi awe na wigo mdogo wa kufanya kazi na kumaliza, lakini tukiwa tunajenga uwezo wa watu wetu wa ndani kuweza kila mmoja kupata kazi na kumaliza kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile tunahakikisha kwamba hakuna anayeuziwa nguzo, Mheshimiwa Waziri atakuja kulisisitiza na kuliweka vizuri. Pia tunaunganisha wateja kwa gharama ya shilingi 27,000 peke yake, Mheshimiwa Waziri atakuja kulisema.

Mheshimiwa Spika, lakini tutahakikisha kwamba katika hiki kipindi cha kupeleka umeme kwenye awamu ya tatu, mzunguko wa pili, tunafungua madawati ya malipo katika maeneo ya wananchi wenyewe. Mtu asifunge safari kufuata sehemu ya kwenda kulipia kilometa 20, 30; madawati ya wenzetu wa TANESCO yatakuwa katika Kijiji au kitongoji ambapo mradi unafanyika. Ilishaelezwa Mheshimiwa Waziri naamini atakumbushia kwamba tutaruhusu hata kulipa kidogo kidogo kwa utaratibu ambao mwananchi atakuwa anaweza ili mwisho wa siku ile shilingi 27,000 iweze kufikia hatua ambayo sasa anaweza kila mmoja akaimudu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunafurahi kwamba TPDC imefanya kazi kubwa, asilimia 60 ya umeme tunaouzalisha unatokana na gesi yetu tunayozalisha ambayo inasimamiwa na TPDC. Hilo ni jambo la kujivunia sana.

Mheshimiwa Spika, katika kipindi hiki tunalo bomba la mafuta limezungumzwa hapa, tunazo fursa kedekede zitakazo kuja. Pia tunafikisha Gridi ya Taifa katika maeneo ambayo hayakuwa na grid, Mkoa wa Kagera ikiwemo, imeshafika Nyakanazi, Mkoa wa Kigoma tutakwenda mpaka Katavi na ni katika muda mfupi sana tutakuwa tumekamilisha yote hayo.

Mheshimiwa Spika, mawili ya mwisho, Wizara imehakikisha inaweka utaratibu mzuri kabisa chini ya uongozi wa Mheshimiwa Waziri kuhakikisha mkandarasi anampata Mbunge na Mbunge anampata mkandarasi. Tunaamini hilo ni sehemu kubwa ambayo itatuwezesha kujadiliana, kushauriana na kusimamiana vizuri kabisa ili muda utakapofika basi yale tunayo yaahidi yaweze kuwa yamefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho japo siyo kwa umuhimu ninashukuru kwamba wakati haya yote ninayoyasema yanatokea, mimi ni Naibu Waziri kwa hiyo nitakuwa na mimi ninajivunia na historia itakuwa imeandikwa kwangu mimi, kwa familia, lakini na kwa Watanzania wenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maelezo hayo mafupi, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wenzetu mtupitishie bajeti yetu, siyo ndogo ni kubwa, lakini itaweza kufanya yale ambayo mtatuagiza kuyafanya kwa moyo thabiti kama ambavyo mmetusifia na kutusemea vizuri tangu mnaanza na kwa kuendelea kutumwa bila kuchoka kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Watanzania basi wanakipata kile ambacho wanakitarajia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninawasalimu kwa Jina la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

WABUNGE FULANI: Kazi Iendelee.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nami nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupatia nafasi ya kujadiliana na kutoa maoni yetu mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, nimesikiliza michango ya Waheshimiwa Wabunge inaonesha nia njema ya kuisukuma nchi kuweza kusogea mbele kwa niaba ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, nilipata maneno, nimeambiwa ni ya kiarabu, yanayosema: “Yashukurunasu lashukurullah.” Nirudie tena kwa ambao hawakusikia, Yashukurunasu lashukurullah, yaani maana yake, asiyemshukuru binadamu mwenzake kwa wema aliomtendea, hawezi hata kumshukuru Mwenyezi Mungu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuwatendea mema sana Watanzania na kuhakikisha kwamba wanafikia katika ile nchi ya ahadi. Pili, nakushukuru na kukupongeza wewe kwa jinsi ambavyo unaliendesha Bunge letu, nasi wanafunzi wako na Wanasheria wenzako tunajivunia na kuona tulipita kwenye mikono salama kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nawashukuru na kuwapongeza Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia kwa michango yao ambayo nimesema inaonesha kabisa kuwa objective na progressive kwa nia ya kuijenga nchi. Niongeze shukurani na pongezi nyingine kwa wale ambao pengine hawakusemwa hapa; hoja zilizopo hapa zinaihusu Serikali na Serikali inayo watendaji. Siyo watendaji wote wameoza, wameharibika, hawana weledi, ni wezi. Wapo ambao ni wazuri na wanafanya yale mazuri ambayo humu tumekuwa tukimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kutufanyia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wangu niwashukuru na niwapongeze watumishi safi wa Umma na tuendelee kuwatia moyo ili wao sasa wasihamie kwenye lile kundi la wengine ambao tunakubaliana hapa kwamba mwisho wa siku tushughulike nao kisawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie kwenye maeneo matatu yaliyosemwa kwenye Wizara ya Nishati, nikikubaliana na hoja na ushauri wa maeneo mengine ambao umetolewa kwenye taarifa ya CAG na kwenye Taarifa za Kamati. Yale ambayo sitayasema kwa taarifa zilivyo, tunakubaliana na tunachukua ushauri na maoni na maelekezo yaliyotolewa kwenye taarifa hizo.

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze kwenye eneo la kwanza la Symbion. Sitakuwa na mengi sana ya kusema hapa kwenye eneo hili. Mkaguzi amekagua objectively na ametoa maoni yake na yalikuwa matatu. Ameshauri mikataba isimamiwe vyema kwa kuwashirikisha wanasheria; pia ameshauri kabla ya kuivunja, basi tuhakikishe kwamba tunaangalia mapato na hasara za sasa na za baadaye; na pia ameshauri kwamba zile pesa ambazo zimelipwa na Serikali zitizamwe namna bora ya kuziweka kwenye vitabu na hesabu za Serikali ili mikeka ikae vizuri. Hayo ndiyo maoni ya CAG, nasi tunakubaliananayo na tunayafanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, naomba nichangie kwenye eneo la mazuri yaliyotokana na malipo yaliyofanywa baina ya Serikali na huyo aliyekuwa Symbion. Nadhani huko panaweza pakawa panafaa zaidi. Wakati kesi inapelekwa Mahakamani, ilipelekwa ikiwa inadaiwa jumla ya kama Dola bilioni moja na milioni mia tano na zaidi kidogo. Kwa
majadiliano yaliyofanyika nje ya Mahakama, imelipwa kama ilivyosemwa, milioni 153 ambazo zinakwenda kwenye bilioni karibia mia tatu na zaidi kidogo. Kwa hiyo, kwa upande wangu naweza kusema pesa nyingi iliokolewa tofauti na kama tungeendelea Mahakamani na kuwa na mafanikio yasiyokuwa chanya, yaani mafanikio hasi, kwa maana ya kushindwa katika kesi hiyo.

Mheshimiwa Spika, ule mtambo ambao umelipiwa zile fedha, sitaki kusema tumeununua; ule mtambo ambao umelipiwa fedha ikiwa ni maelekezo ya makubaliano, thamani yake kwa wataalamu walioifanya ni karibia Dola 120. Kwa hiyo, kwa kulipa milioni 153, maana yake ni kama tumenunua mtambo. Hizo 153 ndani yake kulikuwa kuna deni la bili za kuuziwa umeme, kuna faini ya kuchelewesha yale malipo ya kulipia umeme na gharama za uwekezaji. Kwa hiyo, ukifanya hesabu ya kawaida, inaonekana kama tulichokifanya kilikuwa ni kitu ambacho ni kizuri kwa maana ya kuokoa pesa ya Serikali, ni kama tumenunua mtambo kwa gharama ambazo zilikuwa zina uhalisia.

Mheshimiwa Spika, mtambo huu wataalamu wameuhakiki na kuukagua kuona unaweza kufanya kazi kwa miaka 15 ijayo mpaka 30 bila kuhitaji matengenezo makubwa. Kwa hiyo, bado ni mtambo ambao uko vizuri na unaweza ukatusaidia kwenye kazi zetu za kuzalisha umeme.

Mheshimiwa Spika, tangu ulipoanza kufanya kazi mwezi wa pili baada ya kuwa umelipiwa mpaka huu mwezi Oktoba mwishoni umeshaizalishia Serikali jumla ya Shilingi bilioni 73 kwa kufanya kazi za kuuza umeme katika muda mfupi huu ambao umefanya kazi. Kwa hiyo kwa hesabu hizo ndani ya miaka kama minne kuanzia tulipolipa ile pesa bilioni 153 za dollar ambazo zimelipwa juzi zitakuwa zimerudi kwenye Serikali na Serikali itaendelea kutumia mtambo huu kwa faida zake.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa tunayo chaangamoto ya upungufu wa maji kwenye vyanzo vyetu vya maji mtambo huu wa Symbion unatumia gesi na hivyo sisi kama Serikali kwa kutumia gesi tuliyokuwa nayo na mtambo wetu tuliyoupata baada ya kumaliza ile kesi nje ya mahakama, tunautumia kupunguza gap la upatikanaji umeme kwa takriban megawatt 112 ambazo zinatoka kwenye mtambo huu. Kwa hiyo kwa ushauri wangu na kwa mchango wangu, nadhani yapo mazuri mengi ambayo mtambo huu unatupatia sisi kama Serikali na ni wa kwetu tunaumiliki sisi wenyewe. Kwa maoni na hoja ya CAG nadhani sasa itoshe tuachane na hii habari tuannze kusonga mbele kwa yale mazuri ambayo yamepatikana kwenye hili eneo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye eneo lingine la Mradi wa Mwalimu Nyerere. Kwa Nchi yetu ya Tanzania katika miradi mikubwa ambayo tunayo na tuliwahi kuwa nayo mmojawapo ni huu wa trilioni sita na bilioni 500 na zaidi. Ni faraja kubwa sana kwa nchi kuwa na mradi kama huu tunaoutekeleza kwa pesa zetu za ndani. Katika hili lazima tuipongeze Serikali.

Mheshimiwa Spika, pesa hizi zinapatikana kwa wakati katika yale maeneo ambapo Serikali ya Awamu ya Sita imehakikisha inalipa pesa kwa wakati bila kuchelewa hata siku moja madai yanapokuwa yamehakikiwa ni katika eneo hili la Mradi wa Mwalimu Nyerere. CAG alipokagua ameona mambo ya kushauri na kusonga mbele na tunayachukua kwa sababu ni ya kuboresha. Nisemee mambo mawili tu kwa haraka haraka kwa sababu naona kengele ya kwanza tayari imegonga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mambo mawili makubwa ambayo naona nichangie kidogo ni kuhusu muda wa kukamilisha mradi. Ni kweli mradi ulianza 2018 na ulitakiwa kukamilika ndani ya miaka mitatu ambayo ilikuwa ni Juni mwaka jana. Juni ilipofika mradi ulikuwa haujakamilika kwa sababu ambazo zinafahamika na zinavutana kati ya pande mbili ya Serikali na mtekelezaji wa mradi. Tulikuwa na options mbili sisi kama wasimamizi, tu-abandon mradi kwa sababu muda umeisha au tuwe weledi na wazalendo tuendelee na mradi kwa ku-extend muda huku tukiendelea kuvutana na kubishana kuhusiana na nani mwenye haki, kwenye nini nani kamchelewesha nani na nani kafanya nini? Busara zilituonyesha tutoe kitu kinachoitwa ex-gratia grants of extra time ya kufanya kazi extension of time wakati tukiendelea na majadiliano mengine, nani amechelewesha nini? Nani anamdai nani nini? Nani anatakiwa kumlipa nani?

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIFACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na wachangiaji wengi hapa Wabunge ambao wamechangia, kuna suala ambalo tunaliona labda kama huyu mkandarasi alikuwa anamaliza Mwezi Juni na amechelewesha mradi na kimsingi yule anaye chelewesha mradi ndiye anaetakiwa kuomba Serikali au kuomba aongezewe muda. Sasa hoja iliyokuja ni kwamba mtu amechelewesha mradi halafu ameongezewa muda, ameongezewa na fedha na wataalam wetu mahiri kabisa waliofanya ule mkataba walikuwepo, Watanzania kabisa wazalendo wamefanya ile mikataba, wakakubaliana kwa ngazi yeyote kwamba mradi utaisha mwezi Juni, sasa hii ya kuongeza muda na kuongeza fedha ufafanuzi wake ukoje labda inakuaje hii? (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri wa Nishati, unaipokea taarifa hiyo?

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, mchangiaji hajatoa taarifa, lakini katika mchango wangu sijasema tumeongeza gharama za mradi na nimesema kuhusu kuongezeka kwa muda wa utekelezaji. Kwa hiyo sijasemea kuhusu kuhusu kuongezeka kwa gharama za mradi.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, nadhani nia ni kwamba kwa sababu hii mikataba ambayo tunaingia kwa maana ya Serikali pamoja na hawa wenzetu ambao tunaingia nao mikataba kwa kutoa huduma mbalimbali, upande wa Serikali inaonekana kwenye mikataba pengine si yote, lakini mingi kuwa inalipa ile pesa ya riba kwa kuchelewesha malipo. Sasa huyu mwingine anapochelewesha yeye, Serikali kwa sababu wataalam wapo na mikataba ipo na yeye upande wake analipa? (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema, mkandarasi ana madai yake kwa Serikali na Serikali ina madai yake kwa mkandarasi na kama tungekaa kwenye kuvutana na kubishana tu-establish nani mwenye haki gani kwanza ndio tuendelee na mradi mpaka sasa mradi ungekuwa umesimama. Kwa hiyo alipoomba extension of time kwa sababu alizozileta na akiomba kuongezewa pesa, tumekataa kumwongezea pesa, tumemwambia kwa sababu tuna madai yetu kwako na wewe una ya kwako kwetu hatuja-resolve. Sasa tutakuongezea muda usiokuwa na hayo masharti ya kuongezewa pesa au kuongezeka kwa kitu kingine, tuendelee kutekeleza mradi kwa sababu pesa tunazo na wakati huo tukiendelea kujadiliana nani mwenye haki ya kupata nini.? Kwa hiyo hakuna ambaye mpaka sasa amemdai na kufanikiwa kwa mwenzake kulipa hela ya ziada na sisi tunachokisema ni kwamba hatutalipa pesa ya ziada kwa sababu tunayo madai yetu kwake tukionyesha yeye ndiyo kachelewesha mradi. (Makofi)

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge wawili mmesimama, hiyo taarifa inahusu ufafanuzi aliotoa? Maana ndicho kinachoendelea sasa. Mheshimiwa Mpina.

T A A R I F A

MHE. LUHAGA J. MPINA: Mheshimiwa Spika, ndiyo. Mkataba wetu uko very clear, juu ya mkandarasi kuchelewesha mradi anatakiwa kufanya nini? La pili Waziri hapa anatueleza kwamba Mkandarasi ameomba extension of time na Serikali ika-grant extension of time, base ya extension of time waliipata wapi? Kama hawajafanya tathmini ya kazi iliyofanywa na changamoto zilizopo? Utaipata wapi base of extension of time kama ujafanya tathmini?

SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, sasa nimeshawaanbia anayeruhusiwa kuuliza maswali ni mimi. Mheshimiwa Naibu Waziri hoja yako imeeleweka, sasa haya maswali ya Mheshimiwa Mbunge, ni maswali, kwa hivyo siyo taariafa. Kwa hiyo endelea na mchango wako wako.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna taarifa nyingine nyuma yako. Mheshimiwa Kigwangalla.

T A A R I F A

MHE. DKT. HAMISI A. KIGWANGALLA: Mheshimiwa Spika, nilipenda kumpa taarifa mchangiaji anayezunguza kwamba wametoa extensions ya muda ex-gratia kwa favor, kwa huruma, lakini kule kucheleweshwa kwa utekelezaji wa Mradi kwa zaidi ya miaka miwili kumesababisha mazingira ya utekelezaji wa mradi huo yabadilike. Kwa mfano; kuchelesha tu tayari kunabadilisha exchange rate ya kati ya dollar na shilingi na hatimaye leo hii wanapomlipa pesa nyingine za kukamilisha huo mradi wanamlipa kwa exchange rate ya sasa na hasara ambayo imeingia ni zaidi ya bilioni 110 kwa kuchelewesha tu. (Makofi)

SPIKA: Haya, ahsante sana. Waheshimiwa Wabunge, hili jambo nilikuwa najaribu kuangalia hapa kwenye hivi vitabu vya Kamati wameandika azimio kwa namna gani, lakini hoja hii imeshawahi kufafanuliwa hapa na Mheshimiwa Waziri na kueleza ule mradi umechelewa kwa sababu zipi? Alitoa maelezo, lakini sasa kwa maelezo anayotoa hapa Mheshimiwa Naibu Waziri ni maelezo ambayo ni mahususi kwa zile hoja ambazo zimejitokeza hapa, lakini kwa maana ya yale maelezo ya jumla kukusu mradi Mheshimiwa Waziri wa Nishati alishawahi kusimama hapa Bungeni na akaeleza sababu.

Sasa sisi sasa hivi ili tujielekeze vizuri tuko kwenye hoja hizi hapa za Kamati na tunataka tufike mahali ambapo mchango wa Serikali kwa sasa na wao wanachangia kama Wabunge, lakini utatusaidia Bunge kuazimia kwenye yale mambo ambayo Serikali hatujaweza kujiridhisha na kile ambacho wanasema. Kwa hiyo anachoeleza Mheshimiwa Naibu Waziri ni kile ambacho kimeibuliwa kama hoja, lakini yale mengine ya jumla hayajaletwa bado na CAG na kwa sababu mradi unaendelea CAG atakuja atuambie tu, halafu kwenye ngazi hiyo ndiyo tutashughulika nayo kama haya tunayoshughulika nayo kwa sasa.

Mheshimiwa Naibu Waziri, malizia mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Eneo lingine ambalo naona nilisemee kidogo ni kwenye gharama za mradi zinazohusiana na mabadiliko ya fedha. Miradi mikubwa kama hii inapotengenezewa mikataba inawekewa component mbili, mara nyingi local component na foreign component kulingana na kile ambacho kitatekelezwa kitatumia gharama zipi kubwa? Kwa ilivyofanyika katika mkataba huu gharama kubwa ya utekelezaji wa mradi huu ni mambo yanayotoka nje ya nchi. Kwa hiyo ilikubaliwa kwamba itakuwa ni asilimia sabini ya malipo yatafanywa kwa dollar na asilimia thelathini yatafanywa kwa shilingi ya Kitanzania, kwa sababu supply na mambo makubwa yanapatikana nje ya nchi. Hivyo wataalam walitafuta njia nzuri na namna bora ya kufanya haya. Walijaribu kuhakikisha haifikii sabini ili tuweze kuokoa exchange rate, lakini kwa mazingira na uhalisia ulivyokuwa na wote mnaufahamu mradi huu hatuna haja ya kurudi huko sana ilionekana ibaki sabini kwa thelathini kwa sababu ya uhalisia.

Mheshimiwa Spika, suala pia la kufanya utaratibu wa aging ni kama ku-secure kufanya insurance ya malipo ya baadaye kwenye exchange rate yalitazamwa yote lakini hesabu hazikuleta faida. Kwa hiyo ilikubaliwa kwamba twende na utaratibu huu. Pia kipindi tunaingia mkataba exchange rate tuliyoi-commit ilikuwa na shilingi 2,224.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Mheshimwa kengele ya pili hiyo, dakika mbili malizia mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniongezea muda. Ilikuwa ni shilingi 2,224 kwa dollar moja. Tangu tumeanza kazi dollar imekuwa ikipanda na kuna muda fulani imefikia mpaka shi2,310.93. Sasa hii pesa bilioni 113 iliyowekwa nilihakikishie Bunge lako na Watanzania haijaliwa wala haijapigwa mtu, ni gharama halisia za mabadiliko ya pesa ambayo hata kwenye biashara zetu za kawaida yanatokea.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho kwa haraka haraka, ukwasi wa taasisi zetu ya TPDC na TANESCO, naomba nipende kutoa mchango wangu katika hili.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Kunti Majala.

T A A R I F A

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na yote anayotueleza, pamoja na ucheleweshaji, pamoja na hizo exchanging rate lakini ikumbukwe kuwa mradi huu ulitakiwa pia utoe CSSR kwa jamii inayozunguka ule mradi, lakini mpaka leo zaidi ya bilioni 190 na hazijalipwa mpaka leo. Kwa hiyo hilo nalo waweze kuliona kama Serikali kwa namna gani mradi huu unavyoendelea kudidimiza Taifa letu kwenye suala hilo la mradi na mradi kutokuwa na tija kwa Watanzania.

SPIKA: Ungelikuwa umeishia hapo kabla ya swali lako ungekuwa umetoa taarifa, sasa umeuliza swali. Haya mchangiaji malizia mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA NISHATI: Mheshimiwa Spika, naomba kumalizia mchango wangu kwa kuzungumzia ukwasi wa TPDC na TANESCO. Kwa mara ya kwanza katika historia chini ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania TANESCO imepewa shilingi trilioni 2.4 kama mtaji na wenzetu wa TPDC wamepewa shilingi trilioni karibia 2.8 kama mtaji kwa ajili ya kuweza kujiendesha. Pesa hizi zimetoka wapi? Serikali imeamua kuchukua jitihada za makusudi za kubadilisha deni lake kwenye Taasisi hizi sasa ibadilike kuwa mitaji. Kwa hiyo yale madeni ambayo Serikali ilikuwa imezikopesha hizi taasisi, lakini inaendelea kulipa yenyewe imezibadilisha sasa ili ziweze kuwa mitaji katika taasisi hizi na hivyo zitakuwa na uwezo wa kujiendesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja.