Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Questions from Hon Fredrick Edwad Lowassa (1 total)

MHE. FREDRICK E. LOWASSA Aliuliza:-

Mradi wa maji wa BN 520 una ziada ya lita milioni 100 kwa mujibu wa wataalam na Mheshimiwa Rais alikubali ombi la ziada hiyo kujumuishwa kwenye mradi:-

Je, ni lini utekelezaji wa ahadi hiyo utaanza?
NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Fredrick Lowassa, Mbunge wa Monduli, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji wa mradi mkubwa wa maji wa BN 520 katika Jiji la Arusha, ujenzi wa tanki la maji eneo la Mlima wa Ngorbob Kisongo umeshakamilika. Tanki hili litahudumia Kata ya Mateves, Olmoti na Monduli (Meserani, Kambi ya Sokoine, TMA na Monduli Mjini).

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali tayari imefanya upembuzi yakinifu wa mradi wa kupeleka maji katika Kata ya Mateves na Monduli (Meserani, Kambi ya Sokoine, TMA na Monduli Mjini). Mradi huo umepangwa kutekelezwa katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2021/2022.

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Serikali inajipanga kutekeleza mradi huo, Wizara kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Arusha inatekeleza miradi miwili ya Lolomsikio na Komolonike ili kuboresha huduma ya maji Mjini Monduli. Miradi hiyo inatarajia kuongeza upatikanaji wa maji Mjini Monduli kutoka mita za ujazo 1,430 ya sasa mpaka 2121 na inatarajiwa kukamilika mwezi Februari, 2021.