Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Supplementary Questions from Hon. Yahya Ally Mhata (34 total)

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali ila naomba yafanyike masahihisho. Ni Mji wa Mangaka, sio Banyaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, maswali yangu mawili ni kama ifuatavyo; la kwanza; kwa kuwa Mradi huu wa kuvuta maji kutoka Mto Ruvuma kwenda Mji wa Mangaka unaanzia Kata ya Masuguru, unapita Nanyumbu, Chipuputa, Kilimanihewa hadi Sengenya ambapo matenki yatajengwa. Swali, je, vijiji vitakavyopitiwa na bomba hili vitanufaika vipi na mradi huu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; tunatambua kwamba mradi huu utachukua miaka miwili na wananchi wa Jimbo langu wana shida kubwa ya maji. Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuwanusuru wananchi hawa wakati wanasubiri mradi kukamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ameuliza, kwa sababu Mradi wa Ruvuma utapita kwenye hizi Kata tano alizozitaja, vijiji vitanufaikaje. Kama tunavyofahamu Sera ya Maji hairuhusu Kijiji cha B kianze kupata maji A kikarukwa. Nipende kusema kwamba vijiji vyote ambavyo mradi huu utavipitia, basi watapata maji kwa sababu lile bomba kuu litaruhusu michepuo kwa vijiji vile vinavyopitiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ameongelea suala la muda mfupi. Mradi huu tunautarajia uchukue miezi 12 na tunatarajia uanze mwezi Mei mwaka huu. Mheshimiwa Mbunge hii kazi itafanyika kwa kasi kwa sababu tayari fedha zipo, hivyo itakuwa ni kazi ya muda mfupi na maji yataweza kuwafikia wananchi wetu kwa wakati. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutenga fedha za kutosha kuweza kukarabati na kujenga wodi ya akina mama katika hospitali ya Wilaya ya Mangaka. Hospitali ile imekwisha, je, Serikali inatuhakikishia vipi upatikanaji wa vifaa tiba katika hospitali ile wakati kazi imeshakamilika? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imetenga bajeti ya kununua vifaa tiba katika hospitali zote mpya za Halmashauri
67. Jumla ya shilingi bilioni 33.5 zimetengwa katika mwaka huu wa fedha na tayari taratibu za mawasiliano kati ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Wizara ya Afya na MSD kuona utaratibu wa kupata vifaa tiba katika hospitali zile mpya unafanyika mapema iwezekanavyo ili vifaa vile viweze kupelekwa katika hospitali zetu mpya za Halmashauri na kuanza kutoa huduma zinazotarajiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mhata na Waheshimiwa Wabunge kwamba hospitali zetu zote na vituo vya afya zilizojengwa, taratibu za kuhakikisha zinaanza kutoa huduma za afya zinaendelea na Serikali inaendelea kwa kadiri ya upatikanaji wa fedha, kutenga fedha za kununua vifaa hivyo ikiwemo Hospitali ya Wilaya ya Nanyumbu.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na andiko la huu mradi pamoja na kujenga bwawa, ni kuhakikisha kunakuwa na mtandao wa maji kutoka kwenye bwawa kuelekea Vijiji vya Lipupu, Maratani, Mchangani A na Malema na baadhi ya Vijiji vya Kata ya Mnanje:-

Swali je, ni lini utekelezaji wa uwekaji wa miundombinu ya maji utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Ahadi hii ya kujenga bwawa katika Kata ya Mikangaula ilitolewa tarehe 28/07/2011 na Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne, Mheshimiwa Mrisho Jakaya Kikwete. Swali langu; ni miaka 11 ndiyo mradi huu unatakiwa kutekelezwa:-

Je, Wizara haioni wakati umefika ahadi ya viongozi wa juu hasa Marais wetu ikachukuliwa kama ni agizo na ikatekelezwa haraka iwezekanavyo, badala ya kusubiri miaka 11 ndiyo itekelezwe? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Mtandao wa maji tunaelekea sasa kwenda kuutekeleza. Katika kutengeneza mabwawa, tunaanza kuhakikisha uhakika wa chanzo cha maji ambapo sasa bwawa limeshafika asilimia 95 na sasa hivi kazi zitakazofuata ni kuukamilisha. Hii 5% iliyobaki kufikia mwisho wa mwezi wa Tano au kabla ya kumaliza mwaka huu wa fedha ni kuona kwamba tunakwenda kusambaza mitandao ya mabomba kuelekea kwa watumiaji wetu wote wa Nanyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa swali lake la pili, amesema mradi umeanza tarehe 28/07/2011. Kama wote tunavyokumbuka, miradi hii kwa kipindi hicho ilikuwa chini ya Halmashauri zetu za Wilaya. Kwa hiyo, wale wenzetu kidogo walishindwa kumaliza miradi hii na ndiyo maana RUWASA ikaanzishwa. Sote tunafahamu RUWASA sasa hivi ina mwaka mmoja na miradi korofi yote kama huu imekuwa ikifanikiwa kwa kuweza kukamilishwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge napenda tu kukuhakikishia kwamba tunakwenda kutimiza ahadi hii kwa kutumia RUWASA na wote tunafahamu namna RUWASA ambavyo wamekuwa wakikamilisha miradi chechefu, kwa hiyo, na mabwawa haya pia yanakwenda kukamilika. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba tufanye masahisho katika majina ya vijiji. Kata ya Mkonona ni Nambunda siyo Nambundu na siyo Waniku.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya masahisho hayo, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa dhumuni la uanzishaji Mfuko huu pamoja na madhumuni mengine ni kuziwezesha vile vijiji vya mpakani kuweza kupata mawasiliano ya simu hasa kuhakikisha ulinzi na usalama wa nchi yetu unakuwepo. Mfuko huu ulianzishwa mwaka 2007, vijiji vile bado vina matatizo makubwa ya mawasiliano. Hivi ninavyoongea hatuna mawasiliano ya simu ya Airtel wala mitandao mingine. Je, wakati mchakato huu wa kutangaza tenda unaandaliwa ni hatua gani za dharura zinachukuliwa hili kuhakikisha vijiji vile vinapata mawasiliano hasa kwa kipindi hiki kigumu ambacho usalama wetu na nchi ya Msumbiji ni mbaya? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, tatizo hili la mawasiliano linakwenda sambamba na usikuvu wa redio yetu ya TBC. Katika Wilaya yangu hatuna kabisa mawasiliano ya TBC. Je, ni hatua gani za dharura Mfuko huu unaweza kuisadia TBC ikasikika ndani ya Jimbo langu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. (Makofi
NAIBU WAZIRI WA MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kuonyesha ukaribu na Wizara yetu kwa kuhakikisha kwamba anatupatia taarifa sahihi ili na sisi tuweze kuzifanyia kazi kadri inavyowezekana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ameongelea vijiji ambavyo viko mipakani, Serikali kupitia Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote tayari imeshafanya utafiti na tathmini ya vijiji vyote Tanzania nzima siyo Nanyumbu peke yake ambapo maeneo yote ya mipakani tunatarajia kuutangaza tenda kwa ajili ya ujenzi na kuhakikisha kwamba tunalinda mipaka yetu yote. Mipaka ya Mtwara, Namanga, Sirari pamoja na maeneo mengine Serikali tunafahamu kabisa kwamba mawasiliano ni jukumu letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nilisema katika jibu la msingi maeneo haya ni yale ambayo mara nyingine hayana mvuto wa kibishara. Ndio maana kupitia Mfuko huu kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema ulianzishwa mwaka 2007 kazi yake mahsusi ni kuhakikisha tunafikisha mawasiliano katika maeneo ambayo watoa huduma wengine hawawezi kufikisha mawasiliano, hilo ni jukumu la Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuuliza swali la nyongeza.

Kwa kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu ina vituo vya afya vinne ambavyo vyote havina gari la wagonjwa; je, ni lini Serikali itatuletea magari ya wagonjwa kwa vituo hivyo vya afya? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimetangulia kujibu katika jibu langu la msingi Serikali kwa kuwa imeendelea kujenga vituo vya afya kwa wingi na Hospitali za Halmashauri automatically tumekuwa na uhitaji mkubwa sana wa magari ya wagonjwa katika vituo vyetu vya afya, lakini pia katika Hospitali za Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, safari ni hatua tumeanza na hatua ya ujenzi wa vituo vya afya sasa tunakwenda na hatua ya kutafuta magari ya wagonjwa. Kwa hiyo, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge Mhata kwamba tutakwenda kuangalia na kukipa kipaumbele Halmashauri ya Nanyumbu ili magari ya wagonjwa yakipatikana tuweze kupata gari hilo kwa ajili huduma bora za afya katika Halmashauri ya Nanyumbu. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, shamba hili la Nangaramo lilianzishwa mwaka 1986 wakati Wilaya ya Nanyumbu ikiwa chini ya Halmashauri ya Wilaya ya Masasi. Ukubwa wa shamba hili ni hekta 5,633; hivi ninavyozungumza kuna ng’ombe 300 tu; vijiji vinavyozunguka shamba hili vina uhaba mkubwa wa mahali pa kulima; vijiji vya Kata ya Kamundi, Mkolamwana, Kamundi na Chekereni vina shida kubwa ya mahali pa kulima hata Kata ya Nangomba, Vijiji vya Nangomba na Mji Mwema vina shida kubwa ya mahali pa kulima.

Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri; je, haoni wakati muafaka umefika maeneo haya ambayo hayatumiki kwa shughuli za mifugo wakaruhusiwa wananchi wanaozunguka vijiji hivi wakalima mazao ya muda mfupi, pale ambapo mtakapokuwa tayari basi mnaweza mkayachukua maeneo yenu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; mwaka 2018 kulikuwa na mgogoro mkubwa kati ya wanakijiji cha Mkolomwana na shamba hili, hali iliyopelekea kijana mmoja kupoteza maisha Bwana Ahmad Swalehe na vijana 36 kupelekwa mahakamani. Kwa kuwa kesi ile imekwisha na vijana wale wameachiwa huru kutokuwa na hatia katika mgogoro huu; nini hatma ya kijana huyu marehemu ambaye amepoteza maisha yake kwenye mgogoro huu, je, Serikali ipo tayari kumlipa fidia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Mhata kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, namuelewa Mheshimiwa Mhata na juu ya jambo la mahitaji ya wananchi wa kata na vijiji alivyovitaja vinavyozunguka shamba letu la Nangaramo. Naomba nichukue jambo hili kwa niaba ya Wizara, tutakutana na Mheshimiwa Mhata na tuweze kukubaliana kwenda katika eneo hili la Nangaramo na kuhakikisha tunakwenda kufanya tathmini ya kuona hiki anachokisema na kuzungumza na wananchi na pale itakapoonekana inafaa tunaweza tukaona namna ya kuweza kuwasaidia wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni hili linalohusu marehemu huyu; jambo hili ni kubwa, naomba nilichukue, atueleze vyema na sisi tutafanya mashauriano ya kuona namna iliyo bora ya kuweza kulimaliza suala hili, ahsante sana. (Makofi)
MHE. ALLY Y. MHATA: Mheshimiwa Spika, kwanza naishukuru sana Serikali kwa majibu mazuri kuhusiana na swali hili, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Kijiji cha Maneme ambapo ndipo yalipo majengo haya kilishaandika barua kukabidhi majengo haya kwa Serikali. Mimi kama mwakilishi wao niliwasilisha barua yao ya kukabidhi hili eneo kwa Wizara. Kwa hiyo, nataka kupata commitment ya Serikali. Ni lini watendaji hawa wa Serikali watakuja ndani ya wilaya yangu ili kuyahakiki majengo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa suala hili la ujenzi wa Vyuo vya VETA liko ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na sisi wananchi wa Jimbo la Nanyumbu tunayo majengo tayari, je, Serikali haioni haja kwa Mwaka ujao wa Fedha majengo haya yakatumika ili wananchi wa jimbo langu wakanufaika?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mhata, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyojibu kwenye majibu yangu ya msingi kwamba tayari timu yangu ya wataalam kutoka Wizara itakwenda eneo hili. Mheshimiwa Mbunge anataka kujua lini, nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwa vile tuko hapa Bungeni na Makao Makuu ya VETA yako hapa Dodoma, nimwombe tu Mheshimiwa Mbunge mara baada ya kipindi hiki tuweze kuonana, twende wote kwa Mkurugenzi wa VETA pale ofisini, twende tukaipange vizuri ili tujue wataalam wetu wale lini watakwenda kwenye eneo hili la kuweza kufanya tathmini ya pamoja na kujua kitu gani cha kufanya kule Nanyumbu.

Mheshimiwa Spika, kwenye eneo la pili, kwamba majengo yapo, kuna baadhi ya miundombinu itahitaji kuongezwa; naomba hili tulichukue tuweze kuangalia katika bajeti ijayo iwapo kama itaturuhusu kuweza kuingiza bajeti ya kuongeza miundombinu katika eneo hili. Wakati tathmini hii ikishafanyika itatupa dira ya wapi tunakoelekea, mahitaji gani yatakayohitajika na ni commitment gani itahitajika ya kifedha kuweza kwenda kuongeza miundombinu kwenye eneo hili. Kwa hiyo hili tunaomba tulichukue tutaenda kulifanyia kazi na baada ya tathmini yetu hiyo tutakutana na Mheshimiwa Mbunge kumwonesha kitu gani tunachoweza kukifanya kwenye eneo hili. Ahsante sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, katika harakati za Serikali kuhifadhi mazingira na maliasili yetu ilihamasisha wananchi kufungua mabucha ya wanyamapori. Wananchi wa Jimbo langu walihamasika na walifungua mabucha tatizo ni upatikanaji wa leseni kutoka Wizara husika.

Je, ni lini wananchi wangu watapatiwa leseni ili shughuli hii ya kuuza nyamapori iweze kuanza ndani ya Wilaya yangu?
NAIBU WAZIRI, MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli Serikali imeendelea kutoa leseni za mabucha kwenye maeneo mbalimbali ya hapa nchini na hizi bucha ni kwa ajili ya wanyamapori. Mwaka wa fedha 2020/2021 tuliweza kutoa leseni zaidi ya 46 na tuna masharti ya namna ambavyo wanapaswa kuomba hawa wafanyabiashara wanaofanya biashara hizi za wanyamapori. Lakini kumekuwa na changamoto ya ukosefu wa wanyamapori wenyewe, kwa maana unapowinda kuna- target ambazo wanazifahamu wawindaji. Sasa kumekuwa na malalamiko kwa wale wenye leseni wanakosa nyama na matokeo yake wanarudisha wanashindwa kuendelea na biashara hii.

Mheshimiwa Spika, nimuombe Mheshimiwa Mbunge kama kuna yeyote ambaye anahitaji leseni, Wizara ya Maliasili na Utalii iko tayari wakati wowote kutoa leseni. Lakini changamoto inayojitokeza ni kwamba upatikanaji wa wale wanyama wenyewe ndiyo changamoto halisi inayojitokeza. Kwa sababu, uwindaji kuna maeneo ambayo tunayatenga lakini inapokosekana basi malalamiko yanarudi kwa Serikali, lakini leseni zipo tunawakaribisha wafanyabiashara wote waje. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto hii ya maji inayokuba mji wa Mpanda inafanana sana na changamoto ya maji katika jimbo langu Nanyumbu. Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitumia takribani shilingi bilioni moja kujenga bwawa katika kata ya Maratani ili vijiji vya Lipupu, Maratani. Mchangani A na Malema viweze kupata maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mradi huu haukufanikiwa na Waziri mwenye dhamana alifika katika jimbo langu na kuahidi kutoa kuchimba visima viwili katika kila kijiji hivi nilivyovitaja.

Je, ni lini ahadi hii ya Mheshimiwa Waziri itatekelezwa ili wananchi katika jimbo hili waweze kunufaika na hii ahadi ya Mheshimiwa Waziri? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahadi ni deni na kwa sababu ameahidi Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana, Mheshimiwa Mbunge ninakuhakikishia mgao ujao visima vitakuja kuanza kuchimbwa fedha italetwa.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Naibu Waziri na Waziri wake kwa majibu mazuri ya Serikali. Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu kwenye Jimbo langu la Nanyumbu, sasa hivi kuna kadhia kubwa ya korongo kubwa ambalo limesababisha wananchi wa Kijiji cha Kiuve wawe kisiwani. Jambo ambalo limesababisha mama mmoja kujifungua kwa sababu ya kushindwa kufika hospitalini kutokana na korongo hilo.

Swali, je, Waziri atakuwa tayari kufuatana nami kwenda kuona kadhia kubwa iliyopo ambayo wananchi wa Kijiji kile cha Chiuve wanashindwa kufika hospitalini kutokana na lile korongo ili tutafuta majawabu sahihi ya wananchi wale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa hiyo changamoto ambayo Mheshimiwa Mbunge ameieleza hapa, alinieleza hata kabla hajauliza hili swali la nyongeza na akawa ananiomba kwamba twende wote pamoja. Kwa hiyo, nafikiri amelileta hapa ili nimthibitishie kupitia Bunge. Nipo tayari kuongozana naye ili tukashuhudie hili eneo na tuweze kupata majawabu ya haraka kuhakikisha tunawasaidia wananchi wa eneo la Chiuve. Ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza. Wilaya hii ya Newala ni kati ya wilaya kongwe hapa nchini na shule zake mfano Shule ya Makukwe II, Nakaako na Babati ni shule ambazo zina hali mbaya na mapaa yake yake yanavuja hivi sasa. Kipindi hiki cha masika, vijana wetu wanasoma katika mazingira magumu sana. Swali la kwanza, Serikali itakuwa tayari kuzifikiria shule hizi katika mwaka ujao wa fedha kuipangia bajeti ya kutosha ili kufanya ukarabati?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; linakwenda ndani ya jimbo langu. Katika Kata ya Mikangaula, Wilaya ya Nanyumbu kuna shule ya Mikangaula ambayo ina wanafunzi 1,500 na kuna darasa lina wanafunzi 300. Kwa kutambua adha hii wananchi wa Kata hii wameamua kutumia nguvu zao ili kujenga madarasa katika vijiji vingine. Je, Serikali ipo tayari kushirikiana na wananchi wa Kata hii kuipatia fedha ili vijiji hivi ambavyo vimetoa nguvu zao waweze kupata fedha na kuwanusuru wananchi wao? (Makofi) Je, ni lini Serikali itakabidhi majengo yaliyokuwa ya Hospitali ya Muhimbili kwa Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ili kupunguza uhaba wa majengo katika Hospitali hiyo.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu maswali madogo mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli nimweleze tu kwamba Serikali ipo tayari kuingiza katika mpango Halmashauri ya Newala na kuhakikisha hizo shule kongwe zote zinafanyiwa ukarabati. Hapa nimweleze tu Mheshimiwa Mbunge kwamba mpaka sasa hivi tathmini ya awali tumeshapata tathmini ya Shule 750 za Msingi Kongwe ambazo zimejengwa kabla ya mwaka 1950, yaani kabla ya uhuru wa nchi yetu ambazo tunatakiwa kuzifanyia tathmini.

Mheshimiwa Spika, katika mpango wetu ni ndani ya miaka mitano shule zote kongwe nchini tutazikarabati kwa kujenga madarasa mapya, ndiyo maana katika mwaka wa fedha 2022/2023 tuna ujenzi wa madarasa kwenye Shule za Msingi 12,000 nchi nzima kwa ajili ya kwenda kufanya hayo maboresho. Kwa hiyo, tuko tayari kwa hilo ikiwemo na katika eneo la jimbo la Mheshimiwa katika Kata ya Mikangaula ambayo umeianisha kwamba tutaingiza katika mpango na tutawapatia fedha ili kumalizia hayo majengo. Ahsante sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, msimu wa korosho unaanza mwezi wa Kumi. Je, Serikali haioni haja ya kuweka bei dira kwa zao la korosho kama ilivyo mazao mengine kama pamba?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, Yahya Mhata, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika kikao cha wadau tulichokifanya katika Manispaa ya Songea, katika kikao hiki mwongozo uliotolewa na ambao pia Serikali tunausimamia ni kwamba, utaratibu wa zamani wa bei ya korosho utaendelea ambapo ni utaratibu ule wa kulaza sanduku na baada ya hapo bei itakwenda kutangazwa ili mwisho wa siku wakulima waweze kuipata bei yao katika ufunguzi wa sanduku lile. Kwa hiyo, yale ambayo tulikubaliana na wadau na Waheshimiwa Wabunge pia walikuwepo ndiyo sehemu ya utekelezaji ambao Serikali tutausimamia.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali la nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tarehe 6/6/2022 Serikali yetu iliingia mkataba wa ujenzi wa mradi wa maji kutoka Mto Ruvuma kuja Mji wa Mangaka, miezi minne imefika. Naomba kupata kauli ya Serikali, ni lini mkandarasi atakuwa site ili kutekeleza mradi huo?
WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru na nimpongeze Mheshimiwa Mbunge, kweli eneo la Nanyumbu ni eneo ambalo limekuwa na changamoto sana ya maji. Tumesaini mradi huu tarehe 6/6/2022 kama alivyoeleza, kwa sasa tuna-process advance payment kwa Mkandarasi ili kuhakikisha kwamba anakwenda kutekeleza mradi kwa haraka na wananchi wake waweze kupata huduma ya maji safi na salama.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kuishukuru sana Wizara kwa majibu mazuri.

Mheshimiwa Spika, ndani ya Wilaya yangu kuna vikundi vya vijana ambao wamejiunga pamoja katika shughuli mbalimbali za utafutaji na uchimbaji wa madini. Kuna vikundi kama Chugu, Chiswala na wanaapolo group, changamoto walionayo ni ukosefu wa vitendeakazi sahihi vya uchimbaji. Je, Wizara ina mpango gani wa kuwasaidia vijana hawa vitendea kazi ili nao waweze kupata mapato halali ya kuwezesha kujikimu kimaisha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Taasisi yake au Shirika la Madini la Taifa (STAMICO), limeingia makubaliano na Taasisi za Kifedha hapa nchini, ikiwepo benki ya NMB, CRDB, KCB na Benki hizi zimeanza kutoa mikopo ya kuwawezesha wachimbaji wadogo. Hadi sasa zimeshatoa jumla ya Shilingi Bilioni 36 ambazo zimepopeshwa na inaendelea na jitihada ya kuzungumza na taasisi hizi ili waweze pia kutoa msaada wa vifaa.

Mheshimiwa Spika, vilevile Wizara inaendelea kuhakikisha uchimbaji mdogo unaendelea kurasimishwa nchini na katika mwaka wa fedha 2021/2022 tumeweza kutoa leseni za uchimbaji mdogo 6,000. Niendelee kumuomba Mheshimiwa Mbunge, kwamba ahamasishe vikundi katika Jimbo lake, wajipange na waweze kufuatila uwezekano wa kupata mikopo hiyo kupitia mabenki ambayo tumeingia makubaliano nao kupitia STAMICO. Ahsante sana. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru.

Katika Kijiji cha Maneme Wilayani Nanyumbu kuna majengo ambayo yaliachwa na Kampuni ya ujenzi wa barabara na Serikali ya Kijiji iliyakabidhi majengo yale Wizarani.

Je, ni lini Wizara itatekeleza ahadi yake ya kufungua Chuo cha Ufundi katika Wilaya yangu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mhata Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli eneo hili la Mtambaswala ambapo Kampuni yetu ya ujenzi wa barabara ilikuwa na kambi, tayari imekabidhiwa kwa Wizara ya Elimu kupitia Mamlaka ya Ufundi Stadi (VETA). Mwaka jana mwezi Novemba, 2021 timu yetu ya wataalam ilikwenda kufanya tathmini ya eneo lile namna gani tunaweza tukaboresha, kwa maana kwamba ya kufanya ukarabati pamoja na kuongeza baadhi ya miundombinu ili kiweze kufunguliwa.

Naomba nimuhakikishie Mheshimiwa Mbunge tayari tathmini tumeshafanya na tunatarajia katika mwaka ujao wa fedha, eneo lile tutakwenda kulifanyia kazi kuhakikisha kwamba Chuo kile kinafunguliwa. Nakushukuru sana. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, kuna utekelezaji wa maji katika miji 28, ningependa kufahamu ni jambo gani linakwamisha uwezeshaji wa utekelezaji wa mradi huu hadi hivi sasa haujaanza katika miji 28?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya Mhata kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mradi wa miji 28 kimacho unaweza ukaona haujaanza lakini tayari wakandarasi walifika maeneo yote na tayari wanaendelea kufanya kazi ambazo siyo za site lakini kuanzia Februari hii tunatarajia wakandarasi wengi kuja kuanza kuwaona huko kwenye site na kufanya kazi zile zinazoonekana kwa macho moja kwa moja.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya yangu ya Nanyumbu inakabiliwa na njaa kubwa kutokana na shambulio la panya ndani ya Wilaya yangu. Tuliandika barua tupatiwe chakula cha bei nafuu hadi sasa hivi hatuna majibu. Je, ni nini kauli ya Serikali?
NAIBU WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Mhata, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nikimaliza kujibu maswali haya mimi na Mbunge tutakaa nione barua yake imefikia wapi, lakini nataka nimuahidi kwamba nitampelekea mahindi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE NA URATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri aliyoyatoa Naibu Waziri, Mheshimiwa Antony Mavunde, nataka tuweke jambo hili vizuri kuhusiana na suala hili la njaa. Maeneo mengi Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakitoa taarifa kwamba, kuna shida ya upungufu wa chakula na kwa sababu hiyo sisi kwa mujibu ya Sheria ya Maafa, masuala ya chakula au upungufu wa chakula tunayachukulia kama ni maafa. Kwa tafsiri hiyo utaratibu wake ni kwamba, Halmashauri, Mkurugenzi anaandika barua kwa utaratibu wa kuleta kwa Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu kupitia Mkoani, halafu barua ile inapelekwa kwa Waziri Mkuu, kwa ajili ya kupata kibali sasa ili chakula kile kiweze kutolewa.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu unaotumika sasa ni kama kila mmoja anaenda tu kiholela hivi, lakini kimsingi jukumu la kutoa kibali cha kwa ajili ya chakula ya bei nafuu au cha msaada ni jukumu la Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Waziri Mkuu itakachofanya ni kuwaelekeza Wizara ya Kilimo ili Wizara ya Kilimo sasa waielekeze NFRA kwenda kuangalia maeneo ya kupeleka, kuuzia kile chakula au mtu atakayenunua kile chakula na kwenda kukiuza kwa bei nafuu iliyopangwa. Kwa hiyo niwaombe sana ni kutokana na kukiukwa utaratibu huo, ndio maana mambo hayaendi pamoja na kuwa kwamba barua zimeandikwa.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniona. Jimbo la Nanyumbu liko mpakani mwa Tanzania na nchi ya Msumbiji. Sisi sote ni mashahidi kwamba hali ya usalama sisi na ndugu zetu wa Msumbiji siyo nzuri kwa wakati huu. Majibu ya Serikali nayashukuru sana. Sasa swali kwa Mheshimiwa Waziri: -

Je, ni commitment gani ambayo unaitoa kwa wananchi wa Jimbo la Nanyumbu kuwahakikishia kwamba katika mwaka huo ujao wa fedha 2023/2024 watapata Kituo cha Polisi ili kuwa na uhakika na usalama wao na mali zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, commitment ni kiwango cha asilimia mia moja. Kama bajeti yetu itapitishwa mwezi Juni, uhakika ni kwamba Kituo cha Mangaka ni moja ya vituo vilivyopangwa kujengwa katika mwaka wa 2023/2024. Kwa hiyo, huo ni uhakika, naomba Mheshimiwa Mbunge asiwe na wasiwasi, ahsante sana. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, naomba nimuulize Waziri wa Maliasili na Utalii ni lini itafika katika Jimbo langu la Nanyumbu kutatua mgogoro wa mipaka katika vitongoji vya Wanika na Malomba na kijiji cha Mbangala Mbuyuni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge, kabla ya bajeti hii kuisha basi nimuombe tutafute hata weekend moja tuende tukatatue mgogoro huu. Ahsante. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu mwaka 2018 aliahidi kujenga kilometa tano za lami ndani ya Mji wa Mangaka katika Wilaya yangu ya Nanyumbu: -

Je, ni lini ahadi hii ya kiongozi wetu itatekelezwa ndani ya wilaya yangu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nilijibu swali la awali la Mheshimiwa Hussein Amar, Mbunge wa Nyang’hwale, ndivyo ambavyo naweza kumwambia Mheshimiwa Mbunge kwamba ahadi zote zipo katika mpango wetu na bahati nzuri Bunge lako Tukufu kupitia kauli ya Mheshimiwa Rais mlituongezea fedha Ofisi ya Rais ya TARURA.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, sasa hivi angalau tuna wigo mpana wa kuhakikisha kwamba tunatekeleza hizi ahadi za viongozi kwa wakati. Kwa hiyo, nimwondoe wasiwasi kwamba kabla ya mwaka 2025 tutakuwa tumeanza utekelezaji wa ahadi hiyo ya Waziri Mkuu. Ahsante sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, kwanza naomba nichukue nafasi hii kuishukuru Serikali kwa majibu mazuri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, ukisoma ripoti ya CAG ya mwaka 2021/2022 utaona kwamba kuna upungufu mkubwa wa upatikanaji wa vitabu mashuleni licha ya kwamba Serikali imepeleka fedha katika wizara husika. Kwa mfano ukiangalia Halmashauri Biharamulo ilikuwa na upungufu wa asilimia 45 katika ripoti ya CAG. Ukiangalia Halmashauri ya Bunda takriban vitabu 194,000 havikuwasilishwa mashuleni pamoja na kwamba Serikali imetoa fedha. Sasa je, Serikali haioni kuna haja ya kuzipatia fedha hizi shule husika ili wao wakagiza moja kwa moja kwa wazabuni badala ya utaratibu uliopo sasa hivi fedha hizi kwenda kwenye wizara ambao umekuwa na mlolongo mkubwa sana?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; uwiano kati ya kitabu na mwanafunzi sasa hivi ni kati ya kitabu kimoja wanafunzi watano tofauti kabisa na malengo ya Serikali moja kwa moja. Je, Serikali ina mpango gani wa dharura hasa katika zile halmashauri za pembezoni kuondokana kadhia hiyo katika hoja ya vitabu?
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Ally Mhata Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyoeleza kwenye majibu yangu ya swali la msingi, kwamba Serikali hainunui vitabu badala yake Serikali kupitia TET inaratibu zoezi zima. Kwanza inatunga, inachapa na baadaye kusambaza. Gharama zinazotumika ni zile za kuhakikisha kwamba vitabu vinatungwa, vinachapwa na baadaye kusambazwa kwenye maeneo mbalimbali. Kwa hiyo naomba nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kuwa zoezi hili kupitia mamlaka yetu ya elimu TET tutaendelea kuliafanya kwa uaminifu na uadilifu mkubwa kwa sababu ni jukumu letu la msingi kuhakikisha kwamba vitabu vinafika shuleni kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, katika swali lake la pili amezunguzia suala la uwiano wa vitabu ni kweli uwiano wa vitabu bado hatujafikia katika ile ratio ya moja kwa moja lakini naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea na zoezi hili na hivi sasa Serikali imefanya uwekezaji mkubwa pale Mamlaka ya Elimu Tanzania kwa kununua mitambo ambayo yenye uwezo wa kuzalisha vitabu vingi kwa siku ambao utatuhakikishia sasa maene yote ambayo yenye upungufu wa vitabu tunaenda kuwafikia ili kuweza kufikia ile ratio ya moja kwa moja.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo sasa hivi tumeanzisha maktaba mtandao ambayo katika yale maeneo ambayo mtandao upo au TEHAMA ipo vitabu hivi vinaweza kuwa accessed na wanafunzi pamoja na walimu kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Halmashauri yangu ya Nanyumbu imepokea fedha za ujenzi wa Chuo cha VETA, lakini cha kushangaza fedha hizi zimekabidhiwa Halmashauri ya Wilaya ya Masasi ambayo ipo kilometa 90 kutoka wilayani kwangu: Kwa nini fedha hizi zimepelekwa Masasi wakati Nanyumbu yupo mdhibiti ubora ambaye angesimamia fedha hizi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali dogo la nyongeza la Mheshimiwa Yahya Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ni kweli fedha tumepeleka katika FDC ya Masasi na hatukupeleka kwenye Wilaya ya Nanyumbu moja kwa moja kwa sababu FDC Masasi ndipo ambapo fedha tutazipitishia pale. Tumeona ni muhimu kupitishia hizo pesa pale baada ya kufanya study ile ya ujenzi awamu ya kwanza; Vyuo vyote vya FDC wamesimamia vizuri zaidi vile vyuo vya VETA kuliko zile ofisi zetu za wadhibiti ubora. Kwa hiyo, tumepitisha kule kwa sababu ya kupata usimamizi makini kwa chuo chetu kile na matumizi ya fedha yaweze kuwa sahihi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri, naomba niulize maswali yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza; takwimu ananzozieleza Naibu Waziri sio sahihi. Takwimu ambazo ninazo za waathirika wa wanyama waharibifu ni zaidi ya watu 200.

Je, Waziri yupo tayari kumwagiza Afisa wake aliyopo pale Masasi aende akafanye mapitio mapya ya waathirika wote walioathirika na Wanyama waharibifu hasa tembo katika Kkata ya Sengenya, Kijiji cha Mkumbaru, Chinyanyera, Igunga; Kata ya Nangomba Kijiji cha Chihuve; Kata ya Luimesule; na Kata ya Masugulu? Takwimu hizi sio sahihi kwa hiyo namuomba Waziri afanye hayo kama nilivyomwelekeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili; fidia wanazolipwa waathirika ni ndogo kuliko hali halisi ilivyo. Waathirika hawa wanaopoteza maisha yao fidia ni ndogo, wanaopata ulemavu fidia ni ndogo na wanaoharibiwa mashamba yao fidia ni ndogo. Je, Waziri yuko tayari kuleta Muswada hapa wa kurekebisha viwango hivi ili wananchi walipwe haki sawa kulingana na hali halisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Mbunge kwenye hili suala la takwimu nitazichukua kutoka kwake, lakini pia tutaenda kuhakiki upya katika maeneo hayo ili wananchi waweze kulipwa stahili yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye upande huu wa fidia sheria ya mwaka 2011 iliyopitisha kifuta machozi na kifuta jasho ilikuwa na madhumuni ya kumshika mkono mwananchi, lakini ukiangalia namna ya kufidia mfano maisha ya mwananchi ambaye amepoteza maisha ni ngumu sana kufidia au mtu ambaye amepata ulemavu, hivyo sheria hii ilipitishwa kwa ajili ya kumshika mkono mwananchi kumwonesha kwamba Serikali iko pamoja naye.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo katika Bunge lako hili mwaka jana tulipewa maelekezo ya kuzipitia upya Kanuni zake zinazohusiana na masuala ya kifuta machozi na jasho na hivi karibuni tutaileta katika Bunge lako hili kwa ajili ya kuipitia ili tuweze kuongeza kiwango hiki na Kanuni zirekebishwe, ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Pamoja na kwamba zao la korosho limekuwa likiteremka mwaka hadi mwaka, lakini uzalishaji katika Wilaya ya Nanyumbu umekuwa ukiongezeka sana: Je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kufikiria kujenga kiwanda ndani ya Wilaya ya Nanyumbu ili kuhakikisha kwamba korosho zote za Msumbiji na zile za Wilaya ya Nanyumbu zinabanguliwa pale pale Wilayani?
WAZIRI WA KILIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, siwezi kumwahidi Mbunge mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba tutaenda kujenga kiwanda Nanyumbu. Bali, approach ya ubanguaji tunayoendanayo ni private sector driven, na tunaenda kuisaidia sekta binafsi ya kwetu ya Watanzania. Tutaangalia economic reasons za wapi kiwanda kikae. Kama kutakuwa kuna sababu ya kuweka kiwanda Nanyumbu, tutafanya hivyo, wala hatutasita, lakini kwa hatua ya kwanza, Korosho Processing Center tutakayoanza kuijenga, tutaijenga katika Halmashauri ya Nanyamba na Serikali imeshaanza kulipa fidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama Halmashauri yake inaweza kutenga eneo ambalo tutaanza kuliwekea miundombinu kwa ajili ya baadaye, tuanze huo mchakato sasa hivi, lakini sekta binafsi ndiyo itakayoamua ni wapi inataka kiwanda chake kiwepo, nashukuru. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika,nashukuru, Mkoa wa Mtwara una unganishwa ni Mkoa wa Lindi hadi Morogoro kwa kuanzia katika Wilaya ya Nanyumbu. Barabara hii iko ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Je, ni lini barbara hii itajengwa kwa kiwango cha lami ?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, na kwa kweli tumeongea naye. Hii barabara ni kweli ipo kwenye Ilani. Inapotoka Wilaya ya Nanyumbu kwenda Liwale inapita Selous ambapo inakwenda Ilonga kwenda Mahenge kuunganisha na Mkoa wa Morogoro. Tumeweka kwenye mapendekezo kufanyiwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili kuunganisha Mkoa wa Mtwara, Lindi na Mkoa wa Morogoro kupitia eneo la Ilonga – Mahenge, ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa, Serikali inaniletea majibu siyo sahihi. Barabara niliyouliza mimi ni ya kutoka Mangaka – Nachingwea – Liwale hadi Mahenge, iko ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu. Napatiwa majibu ya Wilaya nyingine ambayo mimi sijauliza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali iko tayari kurudi ikajipange upya iniletee majibu sahihi ya swali langu? Hilo la kwanza.

Swali la pili, barabara ninayoiuliza mimi ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, Mama Samia Suluhu Hassan, alipokuja ndani ya Jimbo langu mwezi Oktoba, 2020. Je, Serikali inatuambia nini juu ya ahadi hii?
NAIBU WAZIRI WA UJENZI (MHE. ENG. GODFREY K. MSONGWE): Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba barabara aliyoisema ya kutoka Mangaka – Kilimarondo ambayo inaunganisha na Mkoa wa Morogoro, sehemu ndogo inahudumiwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, lakini sehemu kubwa inahudumiwa na wenzetu wa barabara za vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakubaliana naye kwamba pia yalikuwa ni maelekezo ya viongozi wa Kitaifa kwamba barabara hiyo ijengwe. Kitu cha kwanza ambacho tutaifanya ni kuipandisha hadhi ile barabara – Mheshimiwa Mbunge atakubaliana nami, kuipandisha hadhi ije TANROADS tufanye upembuzi yakinifu na usanifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilichosema kuhusu barabara niliyoitaja, ni barabara ambazo zinakwenda sambamba, ukitoka Masasi – Nachingwea kwenda Liwale hii barabara inakwenda sambamba na barabara ya kutoka Mangaka – Kilimarondo kwenda Liwale. Sasa hiyo kwa kuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba itapandishwa hadhi halafu itakuja TANROADS tutafanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina ili kuijenga hiyo barabara. Ahsante. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi hii. Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu imechimbiwa visima zaidi ya kumi na tano lakini hadi sasa havijapata pump ya kuendesha visima hivyo. Je, ni lini Serikali itatoa fedha ili visima vyote ambavyo vimechimbwa ndani ya jimbo langu viweze kufanya kazi?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Yahya Ally Mhata kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, visima vilivyoko Nanyumbu tunavishughulikia na manunuzi ya pump yako kwenye hatua za mwisho.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa kunipatia nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwa na migogoro mikubwa kati ya wafugaji na wakulima. Ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu wakulima wa Kata ya Lumesule wana mgogoro mkubwa na wafugaji wa eneo hilo. Hii imepelekea kuhatarisha hata maisha yao. Hivi ninavyozungumza wakulima wako katika hali mbaya sana ya usalama kati yao na wafugaji.

Je, Mheshimiwa Naibu Waziri upo tayari mara baada ya kuahirishwa Bunge letu kesho kutwa, mimi na wewe tukafuatana tukaenda kwenye Kata husika kutatua mgogoro uliopo kati ya wakulima na wafugaji? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MIFUGO NA UVUVI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua kama Wizara iko tayari kuambatana naye baada ya Bunge hili. Wizara iko tayari kuandamana na Mheshimiwa Mbunge. Tuko tayari kwenda kuona mgogoro huu na kuutafutia ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kabla Wizara haijaenda kutafuta ufumbuzi wa mgogoro huu Serikali hii ni kubwa, wapo viongozi ambao wanapaswa kuanza kuhangaika na migogoro hii kabla Wizara haijafika huko. Yupo Mheshimiwa DC, nitoe wito sana, Mheshimiwa DC na wataalam wote waliopo huko wa Mifugo na Kilimo kwenda kutatua mgogoro huu kabla Wizara haijafika huko kutafuta ufumbuzi wa kudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ina Wataalam wa Kilimo na Mifugo, ina Mheshimiwa DC ambaye ni Kamisaa wao. Tunaomba kabla Wizara haijafika huko nitoe wito kwa wakuu wote waende kutatua mgogoro huu kabla hatujafika huko. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba niipongeze Serikali kwa jitihada inazofanya katika kuhakikisha miundombinu yetu inakuwa mizuri, lakini naomba kuuliza swali moja la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika barabara hii ninayoitaja ni ahadi ya Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Tatu, Mzee wetu Hayati Benjamin William Mkapa, ambaye alikuwa Mbunge wa Jimbo hili ambalo mimi nauliza. Sasa ni miaka 25, Serikali bado inatafuta pesa kwa ajili ya kukamilisha barabara hii. Je, Waziri atakuwa tayari katika mwaka huu kuingiza mpango ili mwaka ujao wa fedha, barabara hii ianze kutengenezwa kwa kiwango cha lami? (Makofi)
WAZIRI WA UJENZI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, ningependa nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Waheshimiwa Wabunge kwamba ahadi za viongozi wetu Waheshimiwa Marais Wastaafu na Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, zinatekelezwa, inaweza ikachelewa lakini haimaanishi kwamba hazitatekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameongea kwa hisia kali hapa kwamba ni miaka 25 toka mpendwa wetu Hayati Rais Mstaafu Benjamin Mkapa ameahidi hatujaanza utekelezaji wa barabara hii. Nimhakikishie kwamba, nitafuatilia barabara hii ili hata kama tunaanza kidogo, ilimradi tuanze kutekeleza ahadi za Viongozi wetu, ahsante sana. (Makofi)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi kwenye Wilaya yangu ya Nanyumbu tulipatiwa minara tisa, lakini kuna kata ambayo ina changamoto kubwa haipo ndani ya minara hiyo tisa.

Je, Serikali haioni haja kuleta mnara mmoja kwenye Kata ya Likokona ambayo kuna changamoto ya mawasiliano?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nafahamu kabisa kwamba, Kata ya Likokona ina changamoto hiyo, mimi pamoja na Mheshimiwa Mbunge tulishafika katika maeneo hayo, lakini Serikali ilipokea kata hiyo na katika miradi inayotarajiwa kuja katika ile minara 600, kata hiyo tumeiingiza. Kwa hiyo tumwombe Mheshimiwa Mbunge tuendelee kuiombea Serikali iweze kuendelea kupata fedha kwa ajili ya kuboresha huduma ya mawasiliano nchini, ahsante sana.
MHE. ALLY Y. MHATA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu haya ya Serikali, lakini naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kituo hiki ninachokieleza ni cha muda mrefu sana. Cha kushangaza kituo hiki kililetewa vifaa, vifaa tiba, vyote vya kituo cha afya ambapo kituo cha afya hakijajengwa. Sasa nauliza vile vifaa walivyovileta walikuwa na malengo gani, yaani vitumike wapi wakati kituo hakijafanyiwa ukarabati? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; vifaa vile sasa hivi vimepelekwa katika sehemu nyingine je, Waziri anawahakikishia vipi wananchi wa ile Tarafa kwamba endapo watafanya ukarabati vifaa vile vitarejeshwa pale? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DEOGRATIUS J. NDEJEMBI): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mhata kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, la kwanza kuhusu hiki kituo cha muda mrefu ambacho kimepelekewa vifaatiba, ni wao wenyewe kama halmashauri ambao wanapanga vifaatiba viende kwenye kituo gani cha afya. Kwa hiyo ina maana wao walifanya maamuzi ya kupeleka vifaatiba hivi vipya katika kituo ambacho ni chakavu.

Mheshimiwa Spika, nimtake Mkurugenzi wa Halmashauri ya Nanyumbu kutenga fedha kwa ajili ya kuanza kukarabati Kituo hiki cha Afya kongwe cha Nanyumbu wakati bado tunatafuta fedha. Nitakaa na Mheshimiwa Mhata kuona ni namna gani tunaweza tukapata fedha ya kupeleka kukarabati kituo hiki cha afya.

Mheshuimiwa Spika, nikienda kwenye swali lake la pili la vifaa hivi tiba ambavyo vimehamishwa kwenda kwenye Kituo cha Afya cha Tarafa nyingine na kuhama hapa Nanyumbu. Katika mwaka wa fedha wa 2023/2024, Serikali imetenga bajeti ya bilioni 112 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Ni jitihada kubwa ya mama yetu Samia Suluhu Hassani, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhakikisha kwamba tunapata vifaatiba kuanzia ngazi ya zahanati mpaka vituo vya afya. Nimhakikishie Mheshimiwa Mhata kwamba tutapeleka tena vifaatiba vingine katika Halmashauri ya Wilaya ya Nanyumbu.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, mkandarasi aliyejenga Mkongo wa Taifa kutoka Mangaka kwenda Mtambaswala kwenye kituo cha Mtambaswala imegundulika ameweka vifaa vya zamani na alitakiwa ajenge tank la maji jambo ambalo hakufanya hivyo. Nini kauli ya Serikali juu ya mkandarasi huyu?
NAIBU WAZIRI WA HABARI, MAWASILIANO NA TEKNOLOJIA YA HABARI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ally Mhata, Mbunge wa Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kabisa tumejenga kilometa 72 kutoka Mangaka mpaka Mtambaswala na Mheshimiwa Mbunge tulikuwepo wote wakati tunafika katika kituo kile ambacho ndio kinaenda kuunganisha na Msumbiji. Changamoto ambazo zimejitokeza katika kile kituo tayari Serikali inachukua hatua ili kujiridhisha ni wapi tatizo lilianzia ili kuhakikisha kwamba kituo hiki kinaanza kufanya kazi mara moja, ahsante.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru kwa kupata nafasi hii ya kuuliza swali la nyongeza. Naomba Mheshimiwa Naibu Waziri aweke kumbukumbu sawa ni Jimbo la Nanyumbu, naona maelekezo yako mengi yanazungumza Jimbo la Nanyamba, ni Jimbo la Nanyumbu, liko Mkoani Mtwara na Jimbo la Nanyamba pia liko Mkoani Mtwara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la nyongeza kumekuwa na ucheleweshaji wa fedha hasa kwenye hii miradi ambayo wananchi wanaiibua. Sasa katika Jimbo langu nina maboma zaidi ya Kumi ambayo mpaka sasa hivi hayajapata fedha.

Je, Serikali ina kauli gani juu yama boma hayo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yahya Ally Mhata, Mbunge wa Nanyumbu, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya lengo la Serikali ambalo hata kwenye bajeti tumepitisha, kila mwaka tumekuwa tukitenga fedha kwa ajili ya umaliziaji wa maboma ambayo yameanzishwa huko chini na wananchi pamoja na Serikali zetu kule chini. Kwa hiyo, tumekuwa tukitenga labda kwa kiwango fulani. Sasa hatuwezi kuyamaliza yote kwa wakati mmoja ila kwa wakati. Kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, Mheshimiwa Mhata kwamba hata katika Jimbo la Nanyumbu, tutafanya hivyo katika mwaka wa fedha unaokuja kuongeza baadhi ya maboma ili tuhakikishe yanakamilika yote kwa wakati.
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kuniruhusu kuuliza swali la nyongeza.

Tunayo miradi ya World Bank ambayo ilianzishwa katika Jimbo langu la Nanyumbu, miradi ile ni chechefu; je, Serikali ina mpango gani kuhakikisha kwamba miradi ili chechefu inafanyakazi katika Kata ya Mnanje, Kijiji cha Holola, Kata ya Nandete, Chiwilikiti na Ulanga?
NAIBU WAZIRI WA MAJI: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Nanyumbu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tuna speed kubwa sana ya kuhakikisha miradi yote iliyokaa muda mrefu inakamilika. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais ameendelea kutupatia fedha na tunaona namna kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais kwa kuijali Wizara ya Maji na kuona kwamba akina mama wanatua ndoo kichwani.

Mheshimiwa Mbunge kwenye maeneo haya uliyoyataja tunakuja kuyafanyia kazi. (Makofi)