Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Yahya Ally Mhata (18 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kuchangia katika Mpango huu, naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru sana wapiga kura wangu wa Jimbo la Nanyumbu kwa kura nyingi walizonipatia katika Uchaguzi Mkuu uliopita. Nami nawaahidi wasiogope, niko hapa kwa ajili yao na nitawawakilisha kikamilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijielekeze moja kwa moja katika kuchangia Mpango huu wa Mwaka Mmoja na wa Miaka Mitano uliowasilishwa jana. Kwanza naomba nijielekeze katika sekta ya afya, jinsi gani itakavyoweza kuongeza mapato yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna kitu kinaitwa medical tourism. Tumeona jinsi gani sekta ya afya ilivyoweza kupiga hatua katika miaka mitano iliyopita. Tumeona zahanati karibu 1,198, Vituo vya Afya, Hospitali za Wilaya 99, Hospitali za Rufaa 10 na Hospitali za Kanda tatu. Sasa hospitali hizi zinawezaje kuongeza uchumi wetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukichukulia mfano wa India, wameweza kutumia sekta ya afya kuongeza mapato katika nchi yao. Tunajua wagonjwa wengi walikuwa wanakwenda India. Ni wakati wetu sasa hivi nasi kutumia hospitali zetu kuwavutia wagonjwa kuja katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna balozi zetu katika Afrika. Tutumie balozi zetu kutangaza huduma bora za hospitali zetu. Hawa wakija, watakuja na dola, wataacha katika nchi yetu. Wakija kutibiwa watafanya shopping, wata-stimulate uchumi wetu. Kwa hiyo, ni vizuri balozi zetu zitumike kikamilifu katika kuitangaza nchi yetu hasa huduma za afya ambazo tumeziboresha zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba nishawishi, katika zile wilaya ambazo ni pembezoni, mfano Wilaya yangu ya Nanyumbu tumepakana na Msumbiji, nilitarajia kabisa Hospitali yetu ya Wilaya ikapatiwa vitendea kazi vizuri ili wagonjwa wale wa mpakani waje kutibiwa katika nchi yetu. Wakija watakuja na dola, wataziacha ndani ya nchi yetu na halikadhalika uchumi wetu unaweza kukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni upande wa madini; tumeona jinsi gani Serikali yetu ilivyofanya katika kuhakikisha kwamba katika miaka mitano ijayo inafufua Shirika letu la STAMICO ili kuwawezesha wachimbaji wadogo waweze kujikwamua kiuchumi. Hili eneo la madini ni zuri sana endapo litatumika katika kuhakikisha kwamba vijana wetu wanapata ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya yangu ya Nanyumbu tunayo madini, lakini nina masikitiko makubwa kwamba yameachwa bila kuendelezwa. Wizara ya Madini imefungua duka la ununuzi wa madini, lakini nikawa najiuliza, duka hili linamnufaisha nani? Kwa sababu madini yapo, lakini kuna mgongano mkubwa kati ya Wizara ya Madini na Maliasili. Vijana wanataka kwenda kuchimba madini, wakienda wanakutana na PFS, wanaambiwa hakuna kuingia msituni. Wakienda wanakutana na TAWA, hakuna kuingia. Sasa kuna contradiction hapo, madini yapo lakini hizi Wizara mbili zinagongana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri hizi Wizara mbili zitusaidie vijana wetu ili waweze kufanya shughuli zao, wafuate taratibu gani mahali ambapo pana madini lakini yapo ndani ya msitu? Madini yale lazima yakachimbwe, kwa sababu madini hayapatikani kiholela, hayapatikani barabarani, yapo ndani ya msitu au mbuga. Kwa hiyo, naomba hizi Wizara mbili, nami nawashauri sana, madini haya yasipochimbwa, yatachimbwa kwa njia ya udanganyifu. Kule kwetu mpakani tusipoangalia, wale majirani zetu watakuja kuyachukua na hatutapata chochote. Naomba sana tutumie nafasi hii kuhakikisha kwamba vijana wetu wanapata ajira kwa hizi Wizara mbili kufanya kazi kwa pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kilimo. Kilimo chetu sisi watu wa Kusini hasa Wilaya yangu ya Nanyumbu tunalima sana korosho. Mwaka 2020 tumeathirika sana na uzalishaji wa zao la korosho, lakini Wizara haijaja na majawabu kwa nini zao la korosho halikuzalishwa? Nilitegemea Wizara ya Kilimo itueleze uzalishaji umepungua kwa sababu ya moja, mbili, tatu; vinginevyo tunawavunja nguvu sana wakulima wetu. Wamefuata taratibu zote lakini korosho hazikuzaa na Wizara imekaa kimya. Kwa hiyo, tunategemea Wizara itusaidie.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni ufuta. Tumeuza ufuta kwenye vyama vya msingi, hatujalipwa fedha zetu. Wakulima hawajalipwa. Wizara itusaidie, vyama vya ushirika vinatuangusha. Tunaomba wakulima wale walipwe fedha zao ili iwa-motivate mwakani walime tena.

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema ambaye ameniwezesha jioni ya leo kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu kuchangia hotuba ya Waziri wa Maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri mwenye dhamana na Wizara hii, Naibu Waziri, Katibu Mkuu ndugu yangu Sanga, Injinia wetu wa Mkoa wa Mtwara, Injinia wangu wa Wilaya ya Nanyumbu na watendaji wote wa Wizara ambao kwa njia moja au nyingine wameshiriki kikamilifu katika uandaaji wa bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru mashirika ya dini. Tunalo shirika kule kwetu linaitwa Life Ministry ambao kwa kweli wamechangia sana katika harakati za kupambana na shida ya maji ndani ya Jimbo langu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, shukrani za pekee zimwendee Rais wetu, Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan. Sisi watu wa Nanyumbu tuna kila sababu za kumshukuru sana mama huyu. Tangu ameingia madarakani kuna mapinduzi makubwa ya maji ndani ya jimbo langu. Wananchi wa Kata ya Mikangaula ni mashahidi. Kijiji cha Mikangaula, Kijiji cha Chang’ombe wao walikuwa hawajui maji ya bomba. Tangu mama ameingia madarakani, sasa hivi ninavyozungumza wanakunywa maji ya bomba. Hongera sana mama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kata ya Kamundi Kijiji cha Nawaje walikuwa hawajui maji ya bomba. Hivi ninavyozungumza, kuna DP zaidi ya 10 ndani ya Kijiji. Kwa kweli mama anafanya kazi kubwa sana na sisi watu wa Wilaya ya Nanyumbu tunasema yule anayemsema vibaya mama, alaaniwe. Kwa sababu ameonyesha mapinduzi makubwa sana ndani ya wilaya yetu. Kijiji cha Mkoromwana kulikuwa kuna shida kubwa ya maji leo kuna maji. Ukienda Kata ya Nangomba kuna DP zaidi ya 23. Kijiji cha Nangomba, Kijiji cha Kilimanihewa leo wana maji ya bomba, mambo ambayo huko nyuma hayakuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu, mama anafanya kazi, tuwe wakweli. Leo sisi tunalo bwawa, tuna mabwawa mawili Mheshimiwa Waziri. Ulikuja Bwawa la Maratani tukakushtakia kwamba hapa kuna mchezo mchafu umefanyika ndani ya lile bwawa, ulichukuwa hatua pale pale. Hivi ndivyo inavyotakiwa. Kwa hiyo, nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri na Menejimenti yako yote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Wabunge tunapoleta malalamiko, hatumwonei mtu. Tunazungumza ukweli. Kwa hiyo, nakupongeza sana. Rai yangu Mheshimiwa Waziri, pale Maratani uliahidi kwenye Mkutano Mkuu mbele wa wananchi kwamba kwa kuwa bwawa lile lilichezewa na yule Injinia, kwanza ulimfukuza kazi siku ile, nakupongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia aliahidi kutoa visima viwili kila Kijiji, jambo ambalo mpaka leo halijatekelezwa. Sasa hili Mheshimiwa Waziri nakuomba, kesho utakapokuwa una- wind-up ni kutamka tu vile visima viwili kila Kijiji unatupatia. Wananchi tutakushukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ukienda Kata Nandete kule kulikuwa na mradi mkubwa sana wa maji, nami nilikuomba, hebu leta timu ya wakaguzi, watu wamechakachua ule mradi kule Nandete. Mradi umetumia fedha nyingi, lakini ule mradi hautoi maji ya kutosha. Ule mradi hatutakubali fedha za Serikali, fedha za walipa kodi watu wachache wanufaike nazo, hili jambo halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, tukitoka hapa atoe maagizo watu wakaufanye ule ukaguzi. Holola Kata ya Mnanje kuna mradi wa World Bank. Wananchi pale walijua wamepata mkombozi, lakini ule mradi tangu umezinduliwa haujatoa ndoo hata moja. Naomba waliohusika na ubadhirifu wa ule mradi wachukuliwe hatua. Hili jambo halikubaliki. Muda wa kuchezea maji, muda wa kuchezea fedha za Serikali kwenye miradi ya maji, ndani ya wizara yako, mbele ya wewe Waziri, najua muda umekwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna miradi 28, miji 28. Wilaya yangu ya Nanyumbu ni mmoja wanufaika wa miji 28. Wilaya ya Nanyumbu iko ndani ya Mkoa wa Mtwara. Mimi nasema hongera sana Mheshimiwa Waziri. Mradi huu unatoka Kilometa 65 kuja Mji wa Mangaka. Mahali ambapo bomba litapita kutoka Masuguru kuja Mangaka, vijiji vyote vitanufaika na mradi huu. Hongera sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu, umeongea katika bajeti hapa kwamba unategemea Rais azindue huu mradi. Nakuomba Mheshimiwa Waziri, ufanyike uzinduzi hapa hapa Dodoma kabla Bunge lako hili halijavunjwa. Wabunge wa miji 28 tupo hapa Dodoma, tuwaombe viongozi wetu wa Mikoa wa Chama cha Mapinduzi, viongozi wetu wa Wilaya waje Dodoma washuhudie utiwaji wa sahihi wa miradi hii. Jambo hili litakuwa na manufaa sana na afya sana kwa Chama cha Mapinduzi kwa sababu ndani ya ilani yetu tumeongea bayana, tutatoa maji kwenye miji 28. (Makofi)

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI. Taarifa Mheshimiwa Yahya.

T A A R I F A

MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kumpa taarifa Mheshimiwa Yahya Mhata kwamba mradi huu wa miji 28 tumeuzungumza toka 2016, na ndani yake wamepita Mawaziri sio chini ya wanne. Nami nilishashika Shilingi hapa zaidi ya mara tatu.

Kwa hiyo, kwa kuwa sasa tumefikia hatua ya kusaini na wakandarasi, nami naomba kumpa taarifa kwamba hiyo itakuwa ni heshima kubwa sana, viongozi wa Mikoa hiyo wa Wilaya na Halmashauri hizo kuweko kwenye hiyo signing ceremony na wakandarasi.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Yahya, taarifa hiyo kutoka kwa Mheshimiwa Cosato Chumi.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo kwa mikono yote. Kwa hiyo, ni matarajio yangu kama nilivyosema, jambo hili litafanyika haraka iwezekanavyo ili Wabunge tushiriki na twende tukasimamie utekelezaji wa miradi hii. Kuna watu wanadhihaki, wanasema tunadaganya. Twende tukawathibitishie, muda ule wa uongo umepita, tunataka kazi na kazi iendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati Katibu Mkuu wa Wizara hii, ndugu yangu Sanga, mwezi wa kumi alikuja Nanyumbu. Tulimpeleka kwenye chanzo cha maji cha Masuguru, aliona adha iliyokuwepo. Kwa uchungu mkubwa, ndugu yangu Sanga aliahidi kwenye Mkutano kwamba signing ceremony itakuja kufanyika kijijini hapa mkandarasi atakapokabidhiwa mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. Nami niliahidi…

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Yahya Mhata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aliposema kwamba kuna baadhi ya watu walikuwa wanasema tunadaganya, mwaka 2020 kwenye jimbo langu na Diwani wa Upinzani alikuwa anasema mimi mwongo. Nikawaambia wananchi, kama mimi ni mwongo, mpeni kura. Mkimpa kura, kwenye Kata yenu tutawaondoa kwenye mradi. Hawakumpa kura. Kwa hiyo, wananchi wanasubiri kwa hamu sana maji. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Yahya, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa sababu kuna watu wamezaliwa kwa kusema uongo. Sasa muda wa kuthibitisha uongo wao umefika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katibu Mkuu alipokuja pale Mangaka aliona adha kubwa ya akina mama; ndoo ya maji tulifikia hatua tunanunua kwa shilingi 2,500. Katibu Mkuu kwa uchungu mkubwa alitoa shilingi milioni 100 ili zitumike kutatua tatizo la maji ndani ya Mji wa Mangaka na Kilimanihewa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa uchungu na masikitiko makubwa fedha zile mpaka leo hii hazijatoa matokeo. Nakuomba ukafanye ukaguzi wa ile Shilingi milioni 100. Haiwezekani Katibu Mkuu aje pale, atoe shilingi milioni 100 mwezi wa Kumi, mpaka tunapozungumza leo hakuna hata tone la maji. Cha kuchangaza, jirani kwa ule mradi, kuna mtu binafsi ametoboa na anauza maji ndoo shilingi mia 500.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imetoa Shilingi milioni 100 mwezi wa Kumi mpaka leo hakuna maji. Hiki kitu akikubaliki. Hawa watendaji wanaotuchezea, hatukubali wawe ndani ya wilaya yetu. Ndiyo maana nilimwambia Mheshimiwa Waziri, hii MWANAWASA ni Masasi na Nachingwea, Nanyumbu unahusisha vipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani sisi watu wa Nanyumbu tuwe chini ya Mamlaka ya Mji wa Masasi na Nachingwea. Ndiyo maana tunachezewechezewa kama mpira wa kona. Haiwezekani Unatoa Shilingi milioni 100 kuja kutatua tatizo la maji kwa Mji wa Mangaka na Kilimanihewa, maji hayapatikani. Naomba usipeleke hata senti tano. Kakague kwanza ule mradi tuone matokeo ya ule mradi. Hili jambo halikubaliki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nataka Mheshimiwa leo au kesho utoe kauli, ni lini Wilaya ya Nanyumbu itakuwa na Mamlaka yake ya Maji? Sisi Masasi tunawajibika vipi na Kilometa 54 kutoka Nanyumbu? Hili jambo siyo sahihi. Ile ni Wilaya kamili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Nanyumbu ni wilaya kamili, inajitegemea, ina wataalam wake. Lazima tuwe na mamlaka yetu ya maji ili tuwe na maamuzi ya kufanya. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Naomba yale ambayo nimeyaeleza kesho nitayafuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Yahya.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga sana mkono hoja. Naomba yale ambayo nimeyaeleza kesho nitayafuatilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba kuchukua kuchukua nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipatia nafasi ili kuwa mchangiaji katika Wizara hii ya Maliasili na Utalii. Kama ilivyo ada na mimi naomba niungane na Wabunge wenzangu kushukuru sana na kumpongeza Mheshimiwa Waziri na Naibu wake kwa kazi nzuri wanayoifanya kuhakikisha kwamba Wizara yetu hii ya Maliasili na Utalii inachangia kwa kiwango kikubwa mapato na uchumi wa nchi hii. (Makofi)

Mheshiumiwa Mwenyekiti, kwenye hotuba yake Mheshimiwa Waziri ameeleza kwa kina kwamba Wizara hii inachangia asilimia 25 ya fedha za kigeni na asilimia 21 la Pato la Taifa. Hili jambo ni hongera sana kazeni buti ili mapato haya ya Serikali na Pato la Taifa liweze kuongezeka mara dufu katika mwaka ujao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge tunaimani kubwa sana na Mheshimiwa Waziri, kwa kipindi kifupi ambacho cha miezi mitatu na siku 22 leo juzi ilikuwa siku 19 leo siku 22, kuna mambo mengi umeyafanya ambayo yanaoesha kabisa kwamba umekuja serious kufanya kazi. Ndugu yangu hapa jirani yangu Mheshimiwa Waitara amekubali anasema huyu Mheshimiwa ana kitu ndani yake na mimi nakubali kwamba una kitu ndani yako Mwenyezi Mungu aendelee kukuongoza ili uweze kutumikia Taifa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nampongeza sana Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Wizara hii, ambao mimi najua hawa kwa njia moja au nyingine wameshiriki kikamilifu katika uandaaji wa bajeti hii. Kabla sijaanza kutoa mchango wangu naomba pia nimpongeze sana, sana Mtendaji Mkuu wa TAWA Kanda ya Kusini. Kwa kweli Mtendaji yule anafanyakazi nzuri sana masaa 24 Mheshimiwa Waziri Mtendaji wako yuko kazini. Mimi nilipata majanga makubwa sana ya tembo nilimpigia simu Mtendaji yule alitoa gari yake na Askari wakaja katika eneo la tukio, nampongeza sana Mtendaji yule kwa kazi nzuri anayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nimuombe sana ndugu yangu Waziri, kuna changamoto zipo nyingi ndani ya Wizara yako, nami naomba nizieleze zile changamoto ambazo ziko ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu. Changamoto ya kwanza Mheshimiwa Waziri, ndani ya Jimbo langu kwa mwaka huu tumepata ongezeko kubwa la maafa linalosababishwa na wanyama waharibu hasa tembo. Hili ni jambo la kushangaza haijawahi kutokea ndani ya Jimbo langu watu zaidi ya 200 wamepata mashambulizi na tembo, tembo wameharibu mashamba ya watu, hili jambo kwa kweli linauzunisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kwenye Kata ya Sengenya Mheshimiwa Waziri, vijiji vya Mkumbaru, vitongoji vya Naivanga, Narunyu vimeharibiwa zaidi mashamba 73 ya wananchi yameharibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Kata ya Sengenya pia Kijiji cha Kinyanyila mashamba ya wananchi yameharibika, kwenye Kata ya Sengenya hiyo hiyo KItongoji cha Igunga zaidi ya wananchi 92 mashamba yao yameshambuliwa na tembo. Katika Kata ya Nangomba Kijiji cha Kiuve mashamba zaidi ya 50 ya wananchi yameshambuliwa na Kata ya Kilimanihewa Kata ya Mjini kabisa tuna Kijiji cha Mnonia mashamba ya wananchi yameshambuliwa. Sasa ninachoomba niliwahi kuchangia hapa na nikasema zaidi ya wananchi 200 wameshambuliwa, nina imani Mheshimiwa Waziri majina haya yako ofisini kwako, rai yangu wananchi hawa mashamba ndiyo ajira yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inashangaza sana kuchukua mwaka mzima wananchi kulipwa fidia au kifuta jasho, ni matarajio yangu Mheshimiwa Waziri utachukua kipindi kifupi wananchi hawa waweze kupewa hicho kifuta jasho.

Mheshimiwa Waziri, katika hotuba yako Mheshimiwa Waziri umenifurahisha sana, umekiri kwamba kifuta jasho kinachotolewa ni kidogo na uko tayari kukifanyia marekebisho. Nakuomba Mheshimiwa Waziri, Mwenyezi Mungu akupe nguvu kabla ya Bunge hili hatujamaliza muda wake huu mwezi wa Saba ulete hayo mabadiliko ili wananchi waweze kupata nafuu ya vifuta jasho ambavyo vinasababishwa na hawa tembo. Jambo hili kwa kweli linaudhunisha sana Mheshimiwa Waziri na wananchi watakuombea mema sana endapo utafanya marekebisho haya ya haraka sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo ningependa pia nikuombie ni mgogoro mkubwa uliopo juu ya sekta. Hawa Mawaziri wa kisekta Nane ambao walizunguka Tanzania nzima kutatua changamoto za migogoro. Niliwahi kuzungumza hapa ndani ya Bunge lako, ndani ya Kata ya Mkonona kuna vitongoji vya Chawanika, Kitongoji cha Nambunda na Kitongoji Namaromba, vile vitongoji vimeamuliwa wale wananchi watoke. Mheshimiwa Waziri wananchi hawana tatizo na hilo na tumekubaliana watoke. Changamoto iliyopo wanatokaje?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunavyozungumza ni Mwezi wa Sita wale wananchi ndiyo kipindi cha kuandaa mashamba. Mpaka sasa hivi hawajui watatoka wapi, watatokaje pale na watakwenda wapi? Kwa kuwa tathmini imeshafanyika na maeneo ya kwenda yameshajulikana, walipeni fidia Mheshimiwa Waziri waende huko walikopangiwa, vinginevyo wasipolipwa fidia mwaka huu, mwezi huu au mwezi unaokuja maana yake wale wananchi tunazidi kuwatia umaskini zaidi. Watakwenda wapi kama mpaka sasa hivi hawajui hatma yao?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine wale wananchi pale walipo kulikuwa na shule wameondolewa, shule kule wanakokwenda haijajengwa. Kulikuwa na huduma za maji wale wananchi wangu walikuwa wanatoa maji Mto Ruvuma, walikuwa wanaenda kwa mguu tu kuchota maji, leo wamepelekwa mbali na Mto Ruvuma, kule wanakokwenda wanapataje huduma ya maji? Kule wanakokwenda wanapataje huduma ya afya? Mambo haya yote yangeangaliwa. Sasa mimi ninaomba Mheshimiwa Waziri nina imani na wewe, tufanye haraka iwezekanavyo wananchi hawa waweze kwenda walikopangiwa na hizi huduma muhimu zipatikane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu ni changamoto ya mabucha. Mheshimiwa Waziri Wizara yako ilihamasisha wananchi wale ambao wamezungukwa na hifadhi na mbuga waanzishe mabucha ili kupunguza ujangili na wananchi wetu waweze kupata kitoweo kwa halali. Inahuizunisha wananchi wale mfano mimi kwangu pale, kuna vijana walijiunga Sahachi Company, Sahachi Group walijiunga wakatengeneza bucha, leo ni mwaka wa pili hawajapata kitoweo hata kimoja cha kuuza. Waliuza mara moja tu tena kwa bahati. Sasa Mheshimiwa Waziri, naomba maamuzi yaliyofanywa na Wizara yalikuwa ya busara kabisa ili kupunguza ujangili tuanzishe mabucha ili wananchi wapate kitoweo na wao wawe walinzi wa yale maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kama mpaka sasa hivi hakuna utaratibu mzuri uliopangwa wa kuwawezesha wananchi hawa kupata kitoweo, kwa kweli tunawahangaisha sana. Nina kesi pale kwangu ndugu yangu kuna bwana amehukumiwa miaka mitatu au kulipa faini 500,000 kwa kukutwa na nyama ya nguruwe pori jikoni, amekamatwa jikoni nyama inapikwa nguruwe pori amepigwa miaka mitatu au miezi mitano jela, amekaa jela mpaka ndani ya wiki moja ndugu kuchanga changa wameuza shamba ndiyo kwenda kumtoa. Hii kwa kweli ni unyanyasaji haiwezekani! Hawa Askari wako wanachokifanya siyo sawa, kamateni majangili siyo mtu anayepika, unakwendaje mpaka jikoni? (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri mimi nakuomba hiyo 500,000 nikitoka hapa unirejeshee ili nimpelekee yule mtoto.

MBUNGE FULANI: Kabisa. (Makofi)

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii siyo sawa, siyo sawa hata kidogo na kwa kweli tunawavunja nguvu sana wananchi wetu. Kama wananchi wetu wanalinda maliasili, leo anakutwa na nguruwe pori, mimi kwa kweli jambo hili limenihuzunisha sana, limenihuzunisha sana Mheshimiwa, na ninakuomba sana Mheshimiwa Waziri jambo hili uwakemee sana watu wako. Wanavyofanya siyo sawa na hiyo shilingi 500,000 naiomba ili nimrudishie yule kijana. Wameuza shamba la mikorosho ambalo wamelihudumia kwa miaka 50 lile shamba wameliuza wale wametiwa umaskini, walikuwa na shamba lao sasa wanaingoja TASAF. Maisha gani haya tunawapelekea wananchi wetu? Kwa hiyo hili nakuomba sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nilikuwa naomba sana na mimi nichangie katika masuala mazima ya utalii ni kukupongeza sana katika hotuba yako, umeongea mambo mazuri sana jinsi ya kuboresha na kuongeza utalii na mimi naomba nichangie kidogo. Naomba tutumie Balozi zetu kikamilifu ili ziweze kuchochea utalili wetu. Kule Balozini peleka Maafisa hata Watano kutoka Wizarani kwako, wakawe waambata wa utalii ndani ya Balozi zetu, tusiwategemee Maafisa wa Ubalozi wafanye shughuli ambayo hawana taaluma nayo, peleka Maafisa kule ili wakasimamie shughuli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo najua muda siyo rafiki nitachangia kimaandishi, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote naomba nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambae ameniwezesha mchana wa leo kuwa ndani ya Bunge lako hili Tukufu na kuwa mchangiaji wa kwanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuwatumikia nchi hii. Tatu sina budi kuwashukuru Mawaziri wote wawili kwa uwasilishaji wao mzuri Profesa Kitila Mkumbo kwa uwasilishaji wake mzuri wa Mapendekezo wa Mpango wa Maendeleo kwa mwaka 2024/2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika yale maeneo ambayo yana lengo la kuisaidia Serikali kupunguza nakisi ya urari wa biashara ya nje, hivyo nitajielekeza katika maeneo ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisoma ule uwasilishaji wa Mwenyekiti wa Bajeti ambae aliwasilisha Makamu Mwenyekiti walieleza kwa kina kwamba kilimo cha umwagiliaji ndicho ambacho kinaweza kikaitoa nchi yetu kutoka sehemu tuliyonayo na kwenda sehemu nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika takwimu ambazo amezieleza, wameeleza kwamba nchi yetu ina eneo la hekta 29.8 za kilimo kwa ajili ya umwagiliaji. Hadi Juni, 2023 ni hekta 822 tu ambazo zimetumika kwaajili ya umwagiliaji. Hii inamaanisha kwamba ni asilimia 2.8 tu ya eneo zima limetumika kwa shughuli hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia hizi takwimu utaona kabisa kwamba tuna kazi kubwa ya kufanya. Hatuwezi kuondoa nakisi hii kama hatutatilia mkazo kwenye kilimo cha umwagiliaji. Tunayo mabonde mengi ndani ya nchi yetu, tunalo Bonde kule Ziwa Viktoria, tunalo Bonde la Ziwa Tanganyika, tunalo Bonde la Ziwa Nyasa na tunalo Bonde katika Mto Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo yote haya yanahitaji kuendelezwa ili wananchi wetu, vijana wetu ambao tunawahimiza wajihusishe na shughuli za kilimo waweze kutumia kilimo cha umwagiliaji kama njia ya kujipatia riziki zao. Lakini bila kilimo cha umwagiliaji…

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

MHE. CHARLES M. KAJEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naungana na msemaji sasa hivi kuhusiana na maeneo ambayo yamekuwa identified kwa ajili ya umwagiliaji. Ningeomba wakati Serikali inakuja ku-wind up hebu itutajie maeneo kwamba ni maeneo gani kwa sababu ukisema tu ukubwa bila kutaja maeneo yenyewe mwisho wa siku hatujakua kwamba ni wapi kama tumefanikiwa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa unaipokea hiyo taarifa ya ziada?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea ni mchango mzuri. Kwa hiyo, utaona kwamba kuna maeneo mengi ambayo yanahitaji kuendelezwa kwa kilimo cha umwagiliaji. Mfano katika Bonde la Mto Ruvuma ukianzia Mtwara Vijijini hadi katika maeneo yangu ya Jimbo langu la Nanyumbu eneo lote hili halina eneo kwa ajili ya umwagiliaji jambo hili kwa kweli si sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba Mheshimiwa Kitila Mkumbo waliingize katika mipango ya maendeleo ili vijana wetu ambao tunawahimiza waende wakajishughulishe na shughuli za kilimo waweze kufanya shughuli hii mwaka mzima, vinginevyo watakuwa watu wa kusubiri mvua ya Mwenyezi Mungu ambayo kwa kweli haitaweza kumkomboa kijana huyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali kadhalika ukiangalia vijana wetu wanahitaji nyenzo, nyenzo ambazo zitawawezesha wao kufanya kazi kwa bidii. Changamoto ambayo ipo na ukiangalia ile ripoti iliyotolewa na Kamati ya Bajeti wameeleza mgongano wa kimaslahi kati ya taasisi mbili. Kuna taasisi ya umwagiliaji ambayo ipo chini ya Wizara ya Kilimo, pia kuna bodi inayoshughulikia mabonde ya haya maeneo ambayo iko chini ya Wizara ya Maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo wanawajibika katika kuandaa miundombinu lakini maji ni ya watu wa bonde la maji kwa hiyo matokeo yake mgongano huu unasababisha shughuli za kimaendeleo zisiende mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Mheshimiwa Waziri na Bodi, hebu tukubaliane ni nani anayewajibika uendelezaji wa mabonde yetu haya kwa ajili ya shghuli za kilimo vinginevyo maji yote ambayo yanapatikana yataishia baharini na wananchi hawanufaiki chochote. Naomba sana jambo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni upatikanaji ya mitaji ya kilimo kwa ajili ya wananchi. Jambo hili siyo jepesi kama linavyoonekana, wananchi wetu kwa kweli wanahitaji mikopo. Ukiangalia takwimu ambazo Kamati yetu ya Bajeti imeeleza mwaka 2022/2023 karibu trilioni 2.6 zilitengwa kwa ajili ya utoaji wa mikopo mbalimbali kwa wakulima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kushangaza asilimia Saba ya trilioni 2.6 ilitumika kwa ajili ya mikopo ya uzalishaji na asilimia 93 ilikwenda kwa ajili ya kununua mazao, maana yake asilimia 93 ilitumika kama ulanguzi tu madalali wa ununuzi na asilimia saba peke yake ndiyo ilitumika kwa ajili ya kuwapa watu mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili hatutaweza kutotoa sisi na kuondoa hii nakisi ambayo ipo. Tunahitaji tuzalishe kwa wingi ili tuweza kuingiza fedha nyingi za kigeni. Nitawapa mfano mmoja, mimi natoka ukanda ambao unazalisha sana korosho, mwaka juzi Mkoa wa Mtwara au kwa maana ya korosho yote tulizalisha tani 300,000. Mwaka jana zao la korosho lime-drop kutoka tani 300,000 hadi tani 182,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nini maana yake, maana yake kwamba tumepoteza fedha nyingi za kigeni ukilinganisha mwaka juzi na mwaka jana. Jambo hili kama hatutatilia mkazo tutaendelea kupoteza fedha za kigeni kwa sababu wakulima wetu ambao ndiyo tunaowategemea wazalishe korosho ili tupate fedha za kigeni wanashindwa kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa leo mkulima tunazungumza, mkulima anahitaji mkopo, mtu wa pamba kule anahitaji mkopo kwa ajili ya maandalizi ya shamba lake, mtu wa pamba anahitaji mkopo kwa ajili ya kulipa vibarua ili waweze kuanda shamba lake, mtu wa korosho anahitaji mkopo kwa ajili ya kupalilia mikorosho yake, mtu wa mikorosho anahitaji mkopo kwa ajili ya kununua viuatilifu vya kupulizia shamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imefanya jambo kubwa sana la maana inatoa pembejeo kwa wakulima. Jambo hili nizuri kabisa na mimi naonga mkono mia kwa mia lakini, pembejeo pembejeo peke yake haitamsaidia mkulima. Naomba sana wakulima hawa wapewe mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani leo benki zetu za CRDB, NMB, Benki ya Kilimo hawatoi mikopo kwa wakulima wakati wakulima wote wa Kanda ya Kusini wanahifadhi fedha zao katika hizi benki, hili jambo siyo sahihi! Kama kweli tunataka kuhakikisha tunazalisha Korosho za kutosha na itatuingizia fedha nyingi za kigeni tuwapatie mikopo wakulima wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najiuliza nani mwenye kauli ya kuilazimisha benki hizi zifanye hivyo? Mheshimiwa Hussein Bashe - Waziri wa Kilimo mwaka jana alikaa na hizi benki kwamba toeni mikopo kwa wakulima lakini hakuna benki iliyofanya hivyo! Benki wanakuambia tunashindwa kutoa mikopo kwa sababu wakulima hawalipi, kwa hiyo wale wafanyabiashara walanguzi ndiyo wanapewa hela nyingi lakini wakulima wazalishaji hawapewi mikopo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba sana jambo hili litiliwe mkazo sana ili wakulima wetu waweze kupata mikopo, waweze kuzalisha kwa wingi.

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa.

TAARIFA

MHE. JOSEPH G. KAKUNDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwamba kuna shida upande wa mikopo kwa wakulima hasa vijijini kwa sababu hawana collateral, hii inahitaji mabadiliko ya Sheria ya Ardhi ili watu wa vijijini nao wawe wanapata hati badala ya kuwepa hati nyingine ya kimila ambayo benki haitambui kama collateral.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Yahya unaipokea taarifa?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana na wazo zuri la Mheshimiwa Mbunge. Ni kweli kwamba wananchi wanahitaji mikopo na Serikali ipime ardhi lakini nataka niwaambie kwenye korosho mimi natoka katika eneo la korosho na ni mkulima wa korosho, mikorosho yote wananchi wote mikorosho yao inajulikana na wakulima na mabenki yote yanajua kila mkulima ana hekari ngapi, kwa hiyo inatoa mkopo kulingana na idadi ya mikorosho uliyonayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mkulima anayo account katika benki husika, kwa hiyo hakuna room ambayo itasababisha mkulima ashindwe kulipa huo mkopo. Benki wana sababu ambazo kwa kweli nashindwa kuelewa kwanini hawatoi mikopo kama lengo ni kumuondolea mkulima adha hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu naomba nichangie kipengele cha madini.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Yahya malizia muda wako nimekuongezea dakika moja kwa sababu muda umeisha.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Tumeambiwa hapa kwamba jinsi gani madini yanavyoongezea uchumi nchi yetu, lakini naomba nieleze kuna maeneo ambayo yanayo madini lakini wakati huo huo ni hifadhi za nchi yetu. Je, kuna mpango gani wa wananchi wanaoishi katika maeneo yale ili waweze kuchimba madini yale bila kuadhiri uhifadhi katika maeneo yetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vinginevyo tutakuwa tunalinda yale maeneo tukija kutaharuki madini yote yametoka na wananchi wanakuwa hawana chochote cha kujivunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono na nakubaliana sana na wazo la Mawaziri wetu na nina imani katika mabadiliko haya machache ambayo watayafanya nina imani kwamba tutakwenda pamoja. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumpongeza sana Waziri wa Fedha na Naibu wake kwa kazi nzuri waliyoifanya kuwasilisha mpango huu wa maendeleo wa miaka mitano, mpango wa tatu. Naomba nijielekeze katika njia gani ambazo nazipendekeza zinaweza zikaongeza mapato katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Nchi ya India kabla ya mwaka 2005 ilikumbana na changamoto ya wananchi wake kuhitaji kuwa na uraia pacha. Tatizo hili lilikuwa kubwa, lakini Serikali ya India ilikaa chini na kufikiria jinsi gani inaweza ikatatua tatizo hili na wananchi wake wakaendelea na maisha yao hivyo, wakaanzisha, wakawapatia kitu kinachoitwa Over Seas Citizen of India Card. Kadi ile iliwawezesha raia wote ambao ni wahindi by original kuweza kuingia India kwa wakati wowote na muda wowote wanaotaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kufanya hivi waliweza kutatua matatizo matatu. Kwanza lile takwa la wananchi wa India kuwa na uraia pacha liliondoka kwasababu, lengo lao lilikuwa kuingia India na kushiriki katika shughuli za kiuchumi. Kwa hiyo, kwa kuwapatia hizi kadi za Over Seas Citizen of India raia wa India wanaoishi nchi mbalimbali waliweza kuja India bila matatizo yoyote na ku-maintain uraia wao. Kwa hiyo, Watanzania wengi wenye asili ya India ambao wako hapa Tanzania wanazo kadi hizi Over Seas Citizen of India. Hata raia wanaoishi Uingereza, Marekani, n.k.

Mheshimiwa Naibu Spika, na wahindi hawa wanapofika India wanapata privilege zifuatazo, kwanza wanaweza kushiriki katuika shughuli za uchumi ndani ya nchi ile. Kwa hiyo, wahindi wameweza kuwekeza, wameweza kupeleka uchumi, kupeleka mitaji India kwasababu sasahivi wamekuwa hawana tena pingamizi la kwenda India. Muda wowote na wakati wowote wanaweza kwenda.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili. Raia wa India na huyo ambaye haishi India wana haki sawa. Haki ambazo zinamuwezesha raia wa India, mfano haki za kushiriki katika shughuli za maendeleo, raia wa India na huyo ambaye anakaa nje ya India anafanya wakati mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini waliweka utaratibu wa kuwazuia hawa wenye Over Seas Citizen of India wasifanye mambo yafuatayo; kwanza waliwaambia tunawapatia hizi kadi, hizi sio passport kwa hiyo, wewe sio raia wa India ila tunakutambua kama muhindi mwenzetu. Kwa hiyo, hutaweza kupiga kura katika nchi yetu, hutaweza kushiriki katika shughuli za kiserikali au hautakuwa kiongozi wa kuchaguliwa. Na hautakuwa ukafanya shughuli za kununua ardhi ndani ya India, lakini unaweza ukawekeza katika nchi yetu. Kwa hiyo, India waliweza kuvutia mitaji mingi sana ndani ya nchi yao ndani ya utaratibu huu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nilikuwa naomba tujaribu kuiga utaratibu wa India. Tunao Watanzania wengi ambao wako nje ya nchi yetu wana uwezo na wana pesa za kuja kuwekeza ndani ya nchi yetu. Lakini hawataki kuukana uraia wa hizo nchi. Na sisi hatuna utaratibu wa raia pacha, tuwapatie kadi tuwaite Over Seas Citizen of Tanzania. Wakija hapa waje kwenye shughuli za kiuchumi tu, hata ruhusiwa kupiga kura, hata ruhusiwa kuchaguliwa, hata ruhusiwa kununua ardhi, lakini ataweza kuwekeza ndani ya nchi yetu. Nina imani kabisa tutakuwa na uwezo wa kuwavutia wahindi wengi, waingereza wengi, wajerumani wengi, ambao walikuwa raia wa nchi hii, wamarekani wengi wakaja na wakawekeza ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu huu umewezesha nchi ya India kuinua sana uchumi na vijana wengi wameajiriwa, lakini pamoja na hivyo India waliweza kuvutia teknolojia kwasababu, nchi mbalimbali zilikwenda na wakaweza kuleta teknolojia mbalimbali. Kwa hiyo, halikadhalika kwa nchi yetu nina uhakika kabisa tutakapotumia utaratibu huu tutapata knowledge za mataifa mengine ndani ya nchi yetu; madaktari watakuja kwetu, ma- engineer watakuja kwetu na wataalamu wengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu wa pili ambao naupendekeza, sisi nchi yetu ya Tanzania, natoka Wilaya ya Nanyumbu. Wilaya yangu inapakana na nchi ya Msumbiji. Mheshimiwa Mtenga alipokuwa anaelezea daraja la Mtamba Swala liko ndani ya wilaya yangu. Amezungumzia kutokuwa umuhimu wa lile daraja katika maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lile daraja lilijengwa purposely kwa ajili ya kuinua uchumi wa watu wa Kusini, tatizo ambalo lipo upende wa pili wa lile daraja miundombinu ni mibovu. Naomba sana Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje watumie nafasi hii waishauri Serikali ya Msumbiji waweze kuimarisha barabara kutoka Mtamba Swala kwenda mkoa unaofuata ambao hauko kilometa nyingi. Sasa hivi ninavyozungumza mbao zote zinazokuja Dar-es-Salaam, mbao ngumu, zinatoka Msumbiji zinapitia Daraja la Mtamba Swala. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sisi tunanufaika sana kuwepo kwa lile daraja. Vijana wa Mtwara, vijana wa wilaya yangu wanafanya biashara na mkoa wa jirani wanapeleka mahindi, wanapeleka mchele, wanapeleka samaki, wanapeleka dagaa. Nina imani kabisa endapo miundombinu itaboreshwa upande wa pili wa lile daraja hali ya kiuchumi wa wananchi wetu itaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu naomba sana ndugu zangu viongozi wetu Mawaziri, hawa wawekezaji tulionao tuendelee kuwa-maintain. Kuna tabia ambayo sasa hivi imejengeka, hawa wawekezaji tulionao tunawakatisha tamaa. Tunao wawekezaji wanaofanya biashara ya kuingiza faida, lakini pia tunao wawekezaji wanaotoa huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, kule kwetu tuna Hospitali ya Ndanda tuna Hospitali ya Nanyangao na majirani zetu pale Tunduru wana Hospitali ya Mbesa. Kuna watu wa foreigners wanaoendesha zile hospitali wanapata tabu sana ku-renew vibali vyao. Unashangaa mtu anamkatalia daktari ku-renew mkataba wake; unajiuliza huyu anatafuta nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi nawaomba; hawa watu wanao-renew mikataba ni watalam, na kitendo cha hawa kuwepo wanaongeza utaalam kwa local staffs wetu. Leo unamwambia muda wako umekwisha ondoka aje mwingine. Uapomfukuza yule mtaalam maana yake unaiua ile Hospitali.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa mimi ningeomba, Mheshimiwa Waziri, mama yangu, shemeji yangu, Mama Jenista; hawa wataalam wetu wanatuangusha. Haiwezekani leo unamnyima daktari kuongeza mkataba. Daktari anakataa kuongezewa mkataba wanatutakia mema watu hawa?

Mheshimiwa Naibu Spika, unapomkatalia daktari hata wagonjwa hawaendi tena. Kuna watu wanakuja kwa sababu Doctor Yahya yupo pale. Leo unamwambia rudi kwenu halafu ile hospitali unamuachia nani? Ningeomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie hili, wataalam wetu wanakotupeleka siko, waangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini linguine, kuna baadhi ya missions, mashirika ya dini wanatoa huduma za uchimbaji wa visima. Kuna mashirika kule kwetu wanachimba visima kwenye shule bure. Yule m-mission mkataba umekwisha amekataliwa kuongezwa, anachimbia shule kumi, kumi na tano bure, unamkatalia unapata nini? Amekuja na pesa zake, amekuja na utaalam wake amekuja na vyombo vyake unamwambia muda wako umekwisha rudi kwenu, maana yake wewe hutaki wananchi wetu wapate maji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sana wataam hawa waangaliwe; hasa hawa ambao wanatoa huduma. Mashirika yetu ya dini wana watu wa namna ile wanaanza kufukuzwa eti kwasababu muda umekwisha, jambo hili kwakweli halikubaliki katika uchumi wetu…

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, muda umeisha, …

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba kuchukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu na timu yake kwa bajeti ambayo waliwasilisha jana. Naomba nijiongoze katika maeneo yafuatayo;

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna ahadi ambazo viongozi wetu wa juu wanazitoa ambazo kwa kweli zinahitaji kutekelezwa kwa sababu ahadi ya viongozi hao ni maagizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2011 Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa awamu ya nne alitoa ahadi pale Nanyumbu kujenga kituo cha afya katika Kata ya Mkangaula. Ahadi ile imekuja kutekelezwa mwaka jana. Katika utekelezaji wa ahadi ile zilitolewa milioni 200 lakini milioni 200 mpaka sasa hivi hazijatolewa. Kwa hiyo naomba Ofisi ya Waziri Mkuu, jambo hili liangaliwe katika utekelezaji wa ahadi za viongozi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hiyo haitoshi Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania aliwahi kufika Mangaka tarehe 26/2/2018 na akatoa ahadi ya kujenga barabara zetu za lami kilometa tano; mpaka sasa hivi hakuna hata kilometa moja iliyotekelezwa. Kwa kweli naomba sana, ahadi hizi zinapotolewa wananchi wana imani na viongozi wetu, na zisipotekelezwa tunatoa mashaka kwa wananchi wetu kuwaamini viongozi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mama yetu Rais, Samia Suluhu Hassan alipokuja kwenye kampeni pale Nanyumbu alitoa ahadi ambayo ipo ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya kujenga barabara ya lami itakayounganisha Mkoa wa Mtwara na Morogoro kupitia Seluu; na barabara ile inaanzia ndani ya jimbo langu. Ni matarajio yangu kuwa utekelezaji wa ahadi ile utaanza katika mwaka huu wa fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba sana niungane na Waheshimiwa Wabunge ambao jana walizungumza, kwamba kuwe na kitengo maalum cha kuratibu ahadi za viongozi wetu. Mheshimiwa Rais wetu mpenzi ambaye ametangulia mbele ya haki kuna ahadi nyingi alizotoa, ni matarijio yangu zitatekelezwa ndani ya awamu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna mfuko wa wanawake, vijana, na wenye ulemavu; mfuko huu unategemea mapato ya Halmashauri. Halmashauri nyingi mapato yao ni madogo sana. Wanaonufaika na mfuko huu ni zile Halmashauri ambazo zinauwezo wa kimapato. Lakini mimi concern yangu ipo katika asilimia mbili ya walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ni mlemavu na ni Mbunge wa Jimbo, tunazo changamoto kubwa sana sisi walemavu halafu mnatupangia asilimia mbili, jamani hamtuonei huruma. Ninyi wazima mnaweka asilimia nne na sisi walemavu mnatupa asilimia mbili pamoja na changamoto zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ningeomba kuishauri Serikali, lazima mfuko huu wa wawalemavu uangaliwe na usitegemewe fedha za Halmashauri. Serikali Kuu itenge fedha kwa kila Halmashauri kuwasaidia hawa walemavu.

Mheshimiwa Naibu Spika, walemavu tuna changamoto kwenye elimu. Tunasoma katika mazingira magumu na baada ya kusoma tunategemea tupate ajira. Ukisoma sheria ya ajira kifungu cha 31 (2) ajira za walemavu imeeleza bayana kila mamlaka itakayoajiri watu kuanzia ishirini na kuendelea asilimia tatu wawe walemavu. Najiuliza sheria hii inatekelezwa? Ni kweli taasisi zetu, Wizara zetu zinaasilimia tatu ya walemavu? Na mimi namshukuru sana Mheshimiwa Rais, ndani ya Wizara hii Naibu Waziri ni mlemavu, naamini ataisimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nyingine naomba nijielekeze kwenya afya. Kule Jimboni kwangu kuna mgogoro wa afya. Kuna fedha zilitakiwa ziletwe ndani ya Jimbo langu kujenga kituo cha afya Nanyumbu…

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mhata kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa

T A A R I F A

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimsahihishe tu Mheshimiwa anayeongea pale, asahihishe, watu wenye ulemavu sio walemavu.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Khadija

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Spika, Yes.

NAIBU SPIKA: Toa taarifa yako.

MHE. KHADIJA S. TAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa yangu ni kwamba nataka nimsahihishe kwamba ni watu wenye ulemavu na sio walemavu. Ahsante. (Makofi)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Yahya Mhata unaipokea taarifa hiyo.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana mlemavu mwenzangu amenisahihisha, ni watu wenye ulemavu, na ulemavu ni wa aina zote; nashukuru sana kwa masahisho hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nieleze tatizo la Wizara ya Afya katika Jimbo langu. Tuna kituo cha afya ambacho kilitengewa fedha kwenye Hospitali, kwenye Kituo cha Afya Nanyumbu. Fedha zile hazikuja Nanyumbu, fedha zile kuna mahali zimepelekwa. Uthibitisho wa hili vifaa tiba vikaletwa Nanyumbu; sasa tukawa tunajiuliza vifaa hivi vinakuja kwa hospitali gani? tumeshindwa kuelewa. Kwenye hili naomba Ofisi ya Waziri Mkuu itusaidie. Fedha hizi wamezipeleka wapi kujenga kituo cha afya? kwa sababu tumeletewa machine kwa ajili ya kituo cha afya ambacho hakipo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo nawaomba sana, wananchi wapale wanamasikito makubwa kwamba kuna fedha Serikali yao ilileta kwa ajili ya kituo cha afya lakini fedha zile hazikufika na badala yake waletewa mitambo (machine) kwa ajili ya kituo cha afya ambacho hakijajengwa. Kwa hiyo mimi nina imani kwamba hizi fedha kuna mahali zimekwenda kimakosa, naomba huko zilikokwenda zijereshwe ili wananchi wa Jimbo langu wanufaike na huduma hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba pia nijielekeze katika suala la ufundi ndani ya wilaya yetu tuna majengo yaliyoachwa na kampuni ya kichina ambayo walikuwa wanajenga barabara ya kwenda mpakani Mtambaswala. Majengo yale ni mengi na yapo pale ndani ya Kijiji cha Maneme ndani ya Tarafa ya Nanyumbu; majengo yale yangeweza kutumika kikamilifu kwa shughuli ya elimu ya ufundi. Naomba niishauri Serikali, majengo yale yapo pale idle na yanazidi kuharibika ni bora yakatumika kwaajili ya elimu ya ufundi. Uwekezaji wake hautakuwa mkubwa kuliko kuuanza upya. Kwa hiyo naomba sana wizara inayohusika tuyatumie majengo yale ili kufufua elimu ya ufundi ndani ya wilaya yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho nazungumzia kwenye kilimo. Mheshimiwa Mwambe amezungumza kwamba kilimo chetu kimeathirika sana, uzalishaji wa kilimo wa zao la korosho umeathirika kutoka tani 324 hadi tani mia mbili na kitu, na sababu kubwa zinajulikana na mojawapo ni mbegu bora ambazo tulitegemea wakulima wazitumie hazikutumika. Kwa maana ya Sulphur I mean pembejeo za kilimo na mambo mengine. Wananchi wa jimbo langu walitumia fedha, walitumia nguvu zao kuzalisha mbegu za korosho ambazo miche ile waliwauzia Bodi ya korosho, lakini huu ni mwaka watatu mpaka sasa hivi hawajalipwa pesa zao...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niko

MWENYEKITI: Uko tayari, haya karibu.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri na Naibu wake pamoja na watendaji wote walio chini ya Wizara yake kwa kazi nzuri wanayoifanya.

Mheshimwa Mwenyekiti, tarehe 05 Mei, 2021, niliuliza swali la mawasiliano ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu, Mheshimiwa Waziri alitoa majibu yenye uhakika kwamba tenda inatangazwa na maeneo yote yenye changamoto yatachukuliwa hatua zinazostahili. Ni matarajio yangu kabla hatujaondoka ndani ya Bunge hili nitapata taarifa sahihi tenda imetangazwa lini na nani anakuja katika jimbo langu kufanya kazi hii ya mawasiliano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni changamoto ambayo tumeanza kuishuhudia ndani ya nchi yetu. Wiki mbili zilizopita TRA ilikumbana na changamoto ya mtandao wake wa malipo kutokufanya kazi, karibu siku tatu uchumi wa nchi hii uliyumba, watu hawakulipa na hakuna malipo ya aina yoyote yalifanyika TRA. Siku tatu zilizopita tumeshuhudia Kampuni yetu ya TANESCO imeshindwa kutoa huduma ya kununua LUKU. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni tahadhari, nawaomba sana Wizara, nawaomba sana wataalamu wetu wa TSA wawe waangalifu, dhahama inakuja. Kama hatutakuwa na backup system ya kukabiliana na utaratibu huu iko siku hapa tutakwama kabisa kufanya shughuli zetu. Mheshimiwa Waziri atakapokuja ku-wind-up atueleze ni mikakati gani inayofanywa na Wizara yake kukabiliana na hizi changamoto ambazo zimeanza kujitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni minara. Kuna wajanja ambao wapo ndani ya nchi hii wanapata taarifa kwamba kuna Kijiji A kutawekwa mnara, Kijiji B na Kijiji C. Wanakuja kule wananunua maeneo ya wananchi wetu kwa kujua kwamba kesho unakuja kuwekwa mnara, hawa ni matapeli. Namuomba Mheshimiwa Waziri niko tayari kumsaidia wale wote waliokuja ndani ya jimbo langu wakanunua maeneo ya wakulima kumbe lengo lao ni
kuwekwa minara, minara ile walipwe wahusika. Huu ni wizi mkubwa, haiwezekani mtu atoke huko atokako aje kununua eneo ndani ya kijiji chetu kumbe kesho unawekwa mnara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake Serikali ya Vijiji imekosa mapato, wananchi wamekosa mapato na yule mtu kanunua lile eneo na haonekani yuko wapi. Jambo hili kwa kweli linaumiza sana.

T A A R I F A

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti,

MWENYEKITI: Taarifa.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nataka nimpe Taarifa mzungumzaji, katika Wilaya yangu ya Liwale kuna Kijiji cha Kibutuka kuna tapeli mmoja ameenda kuchukua eneo la shule, mnara uko kwenye eneo la shule lakini unasoma mtu yuko Arusha.

MWENYEKITI: Taarifa hiyo Mheshimiwa.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa hiyo naipokea. Ndani ya Wilaya yangu kwenye Kata ya Sengenya, kwenye Kijiji cha Mkumbaru, kuna hao matapeli wamekuja na wamechukua hayo maeneo na wameweka minara. Kwenye Kata ya Mkonona, kwenye Vijiji vya Mangara Mbuyuni kuna watu wa aina hiyo. Kwa hiyo, naomba sana Wizara ihakikishe kwamba jambo hili kwa kweli linakoma na hawa watu warudishe minara hiyo kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni kuhusu Shirika letu la TTCL. Ni jambo la kushangaza sana inakuwaje Serikali inadaiwa na Shirika hili? Ndani ya bajeti tunapitisha hapa bajeti za Wizara, inakuwaje leo wanashindwa kuwalipa? Hhili jambo halikubaliki. TTCL pia mimi naomba niwalaumu inakuwaje unambembeleza mteja? Kama hakulipi si umkatie? Mbona private sector wanafanya hivyo sisi tunashindwaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja kulialia hapa kumbe power tunazo, tukate. Vinginevyo kama utaratibu huu wa kubembelezana utaendelea mashirika yetu ya umma yatakufa. Tunapitisha bajeti tutalipa umeme, maji, simu, kwa nini wewe Mtendaji Mkuu wa Shirika hukulipa simu TTCL? Unapata huduma bure na unaendelea kuchekewa, hili jambo halikubaliki. Mimi naishauri Serikali, TTCL nendeni mkawakatie wale wote mnaowadai vinginevyo tutakuwa tunakwama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, Shirika letu la Taifa (TBC) matangazo yake hayasikiki maeneo mengi ya nchi yetu. Jimbo letu la Nanyumbu TBC haisikiki kabisa. Mfuko huu wa Mawasiliano kwa nini hawawawezeshi TBC wakasikika nchini kwetu? Hili ni eneo ambalo wananchi wetu wanategemea kupata mawasiliano ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tuko mpakani na Msumbiji, tunatarajia mawasiliano ya uhakika yapatikane kutoka…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante, muda wako umekwisha.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja lakini namuomba Mheshimiwa Waziri jioni hapa hapataeleweka kama hakutakuwa na majibu sahihi. Ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nami naomba nichukue nafasi hii kwanza kuipongeza sana Wizara, kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na viongozi wote wa Wizara kwa kazi kubwa waliyoifanya katika uandaaji wa bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nielezee kwa ufupi faida za korosho. Korosho tunapata tunda, katika lile tunda tunaweza tukatengeneza juice na wine. Lile bibo lilikauka unaweza ukatengeneza spirit, viwandani, hospitalini na kwenye maabara tuna shida kubwa ya spirit. Wenzetu wa Naliendele wamekwenda mbali kutengeneza spirit kwa kutumia bibo. Sasa hivi wamefikia asilimia 82 ya spirit kwa tunda lile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, korosho yenyewe unaweza ukala, wengi wenu mnajua kazi yake lakini unaweza ukatengeneza siagi. Wenzetu wa Naliendele wana siagi ya korosho na imekuwa approved na TBS. Pia ile korosho ukisaga, unaweza ukatengeneza chapati. Aidha, korosho ni tui, unaweza ukapika mboga kwa tui la korosho na ukikutana na mwanamke wa Kimakonde hutamuacha. (Makofi/ Kicheko)

Mheshimiwa Spika, nutshell ya ile korosho ni mafuta yanayotumika katika dawa. Unaweza ukapaka kwenye mbao kama alivyosema mwenzangu na ile haitaliwa na mdudu yeyote. Lile bibo ukishakamua ni mashudu na ni mbolea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niiulize Wizara, mambo haya walikuwa wanayajua? Viwanda vingeitumia korosho hii leo tungekuwa wapi? Nina uhakika tungetengeneza wine…

T A A R I F A

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe taarifa Mheshimiwa Mhata.

SPIKA: Ndiyo Mheshimiwa Cecil.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, napenda kumpa taarifa kwamba pamoja na hayo anayoyasema, Serikali hii ilikamilisha utafiti wa haya yote anayoyasema ambao unapatikana pale Naliendele kinachosubiriwa ni kufanya implementation. Kwa hiyo, sasa awaulize utekelezaji wa haya yote ili kuongezea wakulima mapato kutokana na zao la korosho utaanza lini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nampa taarifa hiyo.

SPIKA: Taarifa hiyo unaipokea Mheshimiwa Yahya?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, huko ndiyo nilikokuwa nakwenda, namshukuru sana mwenzangu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba wenzetu wa Wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Wizara ya Viwanda na Biashara ule Mfuko wa export levy ndiyo ulitakiwa ufanye kazi hizi. Tuna kazi kubwa ya kufufua viwanda vyetu vya wine, kutengeneza viwanda vya mbolea na juice. Kama tungeutumia Mfuko ule vizuri kwa kuwatumia wataalam wetu wa Naliendele, miaka hii mitatu tuliousimamisha tungekuwa tuko mbali sana. Kwa hiyo, naiomba sana Wizara tutumie Mfuko ule wa export levy ili kuwezesha wenzetu wa Naliendele wafanya utafiti wao wa dhati kutafuta mazao mbadala ya korosho hatimaye viwanda vingi viweze kutekelezwa ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala langu la pili, kule Jimboni kwetu kumeingia mtafaruku. Kuna barua iliyoandikwa na Mtendaji Mkuu wa Bodi ya Korosho inayowataka wakulima wote kukatwa Sh.110 kutoka katika mauzo yao ya korosho baada ya kupewa sulphur. Barua ile inachanganya sana. Inasema hata mkulima akipewa mfuko mmoja akienda kuuza tani 20 atakatwa Sh.110 kwa kila kilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mtendaji huyu amekwenda mbali kwa kujiamini kabisa kwa kuwaandikia Wakurugenzi kwamba hayo ni maagizo na lazima yatekelezwe. Hili jambo halikubaliki. Kama mwananchi anakopeshwa mfuko mmoja, kwa nini usimkate kwa mfuko mmoja? Unamkataje kwa idadi ya korosho alizoleta kwa ajili ya kuuza go-down? Hii kitu hakikubaliki.

Mheshimiwa Spika, tunaomba Mheshimiwa Waziri, ile barua ifutwe. Mtendaji yule anasema baraka hizi amezipata kwa Wabunge, Wabunge wapi? Ni nani aliyempa idhini ya kuandika barua hiyo? Kwa kweli anatuchanganya na anawachanganya wananchi. Namuomba sana Mheshimiwa Waziri, Mtendaji huyu usipomuangalia ipo siku tutamtoa ofisini kwake kwa nguvu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la minada, Mheshimiwa Waziri amezungumza vizuri sana asubuhi kwamba takriban minada 70 imefanyika ndani ya nchi hii kwa msimu uliopita na minada ile ni mizuri kabisa na mimi naiunga mkono. Hata hivyo, kuna upungufu kwenye minada ile.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Tandahimba imetokana na Wilaya ya Newala lakini utashangaa bei za minada zinatofautiana. Unaambiwa korosho za Tandahimba ni bora kuliko korosho za Newala ambapo jana walikuwa Wilaya moja. Leo kwa kugawanywa tu, bei zinatofautiana. Wilaya ya Nanyumbu, wilaya yangu mimi imetokana na Wilaya ya Masasi. Mwanzo, bei ilikuwa moja kwa kugawanywa tu, bei zinatofautiana, hii ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri uwaangalie watendaji wake kuna hujuma inayofanyika. Haiwezekani korosho za Nanyumbu zikawa na bei ndogo kuliko korosho za Masasi. Wakati tulikuwa wilaya moja bei ilikuwa sawa, leo tunagawanywa, unasema kwamba bei tofauti. Hili jambo halikubaliki. Kwa hiyo, kuna hujuma inayofanyika na haitakubalika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niishauri Wizara, pamoja na mazuri yote wanayoyafanya, naomba muwaangalie watendaji wenu wa chini. Wenzangu wamezungumza kuhusu Bodi ya Korosho, mtendaji amepewa mamlaka makubwa sana kwa sababu hana mtu anayemdhibiti. Naomba huyu mtu aangaliwe kwa macho mawili. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Yahya.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, mwisho naishukuru sana Wizara naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, na mimi naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Balozi Mulamula kwa kuwasilisha vizuri sana na kwa umahiri mkubwa bajeti ya Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki. Lakini pia naomba nichukue nafasi hii kuwashukuru watumishi wote wa Wizara hii kwa ushirikiano walioutoa katika uandaaji wa bajeti hii.

Mheshimiwa Spika, naomba pia nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa maono mazuri aliyonayo juu ya Wizara hii. Kwa mara ya kwanza Wizara hii inaongozwa na wabobezi wa diplomasia, hakuna atakayebisha Waziri wetu ni mbobezi hakuna atakayebisha, Naibu Waziri ni mbobezi hata Katibu Mkuu wa Wizara hii ni mbobezi katika masuala ya diplomasia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mimi sina mashaka na watu hawa na namshukuru sana, sana, sana Mheshimiwa Rais kwa kuliona hilo. Wakati Rais wetu analihutubia Bunge baadhi ya maneno ambayo aliyazungumza katika Wizara hii ni kama ifuatavyo na naomba ninukuu alisema; “tunafanya uchambuzi utakaobaini nafasi ya kila ofisi ya Ubalozi katika kukuza biashara, uwekezaji na utalii, uchambuzi huo ndio utakaotumika kupanga Maafisa kulingana na uwezo wa kila Balozi.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nakuja kwenye mchango, tunazo changamoto nyingi sana katika balozi zetu,

Mheshimiwa Rais ameeleza hapa. Bahati nzuri mimi nimewahi kufanya kazi katika balozi zetu, nilikuwa Ubalozi wa Tanzania New Delhi, India ni jambo la kushangaza Ubalozi ule una watumishi watatu ambao wanawakilisha ukiondoa India kuna nchi zingine za uwakilishi. Hapa unajiuliza diplomasia ya kiuchumi utaitekeleza vipi kwa idadi hii ya watumishi. Kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri maelezo yale ya Mheshimiwa Rais ayafanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na nimuombe Mheshimiwa Waziri aangalie umuhimu wa India kimkakati katika kukuza biashara, kimkakati katika masuala mazima ya utalii. India ndio makao makuu au ndio soko letu kuu la korosho zote zinazotoka Tanzania. Kuna Jimbo linaitwa Kerera, korosho zote za dunia hii zinakwenda pale, kwa hiyo, lazima tuwe na watumishi wa kuhakikisha wanalikamata soko lile. India ndio makao makuu ya textile industry ukienda Jimbo la Gujarat, ndio pamba yote inayozalishwa duniani inakwenda kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, India ndio makao makuu ya matibabu, ukiwa na tatizo la kiafya usipopona India wewe ujue huponi tena. Kwa hiyo, kuna kila sababu kuhakikisha tunapeleka watumishi wa kutosha wa kuweza kuhakikisha kwamba tunaweza kupata wawekezaji wa kutosha ambao watakuja kuisaidia nchi yetu. Lakini hali ilivyo sasa inatia huzuni sana haiwezekani nchi kama India sub-continent unakuwa na watumishi watatu, ambao unatakiwa utoe huduma Srilanka, utoe huduma Bangladesh na utoe huduma na Napal jambo hili haliwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, namuomba sana Mheshimiwa Waziri aangalie maelekezo ya Mheshimiwa Rais kuna kila sababu ya kujipanga kimkakati katika kuhakikisha kwamba tunawapanga watumishi wetu kwa lengo zima la kukuza biashara zetu, kukuza utalii wetu na kukuza uchumi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tuna suala la rasilimali watu, nimelizungumza upungufu wa watumishi na jambo hili kwa kila mahali ukienda China, kuna watumishi watatu Balozi na watumishi wawili, mwambata wa jeshi na mwambata wa fedha hauwezi ukafanya kazi kwa kuleta tija katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini suala la maslahi ya watumishi; unaweza ukawaona watumishi wa Ubalozini wanapata maslahi makubwa kweli jambo hili si sahihi. Bara la Asia watumishi hawa wamegawanywa kimatabaka, mtumishi aliopo New Delhi, India analipwa tofauti na mtumishi aliyopo China. Mtumishi aliyopo China analipwa tofauti na mtumishi aliyopo Malaysia, kwa nini watumishi hawa tunawapa allowance tofauti? Ningeshauri Mheshimiwa Waziri ili kulinda maslahi ya watumishi tuhakikishe watumishi wetu tunawapa maslahi yaliyosahihi na yanayolingana. Haiwezekani Balozi wa India analipwa tofauti na Balozi wa China, analipwa tofauti na Balozi wa Malaysia wakati hawa wote ni Mabalozi, hawa wote ni watumishi walioko katika nchi zetu kwa hiyo, naomba maslahi ya watumishi yaangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kingine watumishi waliopo Ubalozini hawalipwi stahili zao, takribani miaka kumi hakuna mtumishi wa Ubalozini anayelipwa fedha ya likizo, watumishi hawa inabidi wajitegemee wao wenyewe jambo hili kwa kweli linakwamisha sana ustawi wa kazi zao.

Mheshimiwa Spika, lakini imeelezwa hapa changamoto ya makazi ya watumishi, naomba niishauri Wizara naomba tutumie mifuko yetu ya Hifadhi ya Jamii tuliyonayo ikajenge nyumba katika Balozi zetu, kwa kufanya hivi tutakuwa tumefanya mambo mawili, kwanza tutaisaidia Serikali kutoa fedha kwa kujenga nyumba lakini pili, tutarejesha fedha zetu hapa hapa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama utawaambia National Housing waende Nairobi wakajenge nyumba, nyumba ambazo watumishi wa Ubalozi watakaa, maana yake Wizara ya Fedha itailipa National Housing. Kama utawaambia National Housing wakajenge nyumba India maana yake watumishi wa Ubalozini watakaa katika nyumba za National Housing na Wizara ya Fedha itailipa National Housing, kwa hiyo, tutaacha fedha zetu ndani ya nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na kwa kufanya hivi tutajenga nyumba nyingi sana, lakini kama tutaendelea na utaratibu wa kumbana ndugu yangu Mwigulu atoe fedha Hazina, tutakesha hatutamaliza tatizo la nyumba.

Mheshimiwa Spika, kuna mjumbe hapa amezungumzia masuala ya raia pacha, niliwahi kuzungumza ndani ya Bunge hili kwamba tatizo hili liliwakuta wenzetu wa India, lakini walilimaliza kwa utaratibu mzuri sana. Badala ya kutoa uraia pacha, wao waliwatambua raia wao waliopo nje ya nchi kwa kuwapa kadi, wanaitwa Non-residence of India (NRI) na sisi tuwatambue Watanzania waliopo nje ya nchi tuwaachie na uraia wao lakini tuwape kadi Non-residence of Tanzania. (Makofi)

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, kwa kufanya hivyo…

SPIKA: Nimekuona Mheshimiwa Mbunge wa Longido.

T A A R I F A

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi nimpe mzungumzaji taarifa kwamba katika Taifa la Marekani pia wanawapa wageni green card kuwatambua kwamba wanaweza kuishi na kufanya kazi huko.

SPIKA: Unapokea jambo hilo?

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nashukuru naipokea taarifa hiyo. Kwa hiyo, ninachojaribu kueleza hapa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana bahati mbaya na muda wako umeishia hapo hapo.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kuweza kunipa nafasi hii nami kuweza kuchangia bajeti hii ya Serikali.

Awali ya yote naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Mama Samia Suluhu kwa maono mazuri aliyonayo juu ya nchi yetu, pili nimshukuru sana Waziri Dkt. Mwigulu Nchemba, Naibu wake na wafanyakazi wote wa Wizara ambao kwa namna moja au nyingine wameshiriki kikamilifu katika uandaaji wa bajeti hii. Tatu, naomba niwashukuru sana Mwenyekiti wa Kamati yetu ya Bajeti, Ndugu yangu Mheshimiwa Daniel Silo, Makamu wake CPA Omar Kigua kwa mchango mzuri walioutoa kwenye Kamati na kuishauri Serikali hatimaye leo hii tunaijadili bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichangie katika maeneo yafuatayo, kwanza naipongeza sana Serikali kwa maono yake iliyonayo juu ya kuhakikisha Madiwani wetu wanapata posho moja kwa moja kutoka Serikali Kuu. Tatizo hili lilikuwa tatizo kubwa sana, Rais wa Awamu ya Nne Mheshimiwa Dkt. Jakaya Kikwete alifanya kama leo Mama yetu anavyofanya, aliamua kuhakikisha Madiwani wote wanalipwa kiinua mgongo kutoka Serikali Kuu, hii ilikuwasuluhisho la matatizo kwenye Halmashauri zetu. Leo hii tunapoamua kuwalipa madiwani posho zao kupitia mfuko mkuu tunahakikisha Halmashauri zote tunazitendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana posho inayopatikana sasa hivi ni ndogo. Mheshimiwa Waziri kwa kuanzia ajaribu kuona alternative way ambayo tunaweza tukainua kidogo posho za Waheshimiwa hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwangu Mheshimiwa Diwani anahudumia vijiji 12, anatembea ana vijiji 12. Nina Kata mimi inaitwa Kata ya Sengenya Mheshimiwa Diwani ana vijiji 12, posho hii yote anayopata inatumika katika kuhudumia vijiji hivi. Kwa hiyo, badala ya kutumia kidogo kujikimu anajikuta anaitumia kwa ajili ya shughuli za wananchi. Kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri hili aliangalie. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza sana Serikali kwa kuamua kuwalipa Maafisa Watendaji wa Kata posho zao, posho za mafuta. Pamoja na kwamba, Maafisa Watendaji hawa hawana vitendea kazi, lakini ninaamini wataitumia posho hii kwa ajili ya kukodi bodaboda, ili kuweza kufanya shughuli za halmashauri. Sisi ni mashahidi, sisi ni Madiwani, tunafahamu Maafisa Watendaji Kata wetu ndiyo wakusanya ushuru wa Halmashauri, ndiyo walinzi wa amani katika Halmashauri zetu kwa hiyo, kwa kweli, hizi 100,000/= watakazopewa zitawasaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu hii isiwe hisani, Wakurugenzi wa Halmashauri wasije wakawakopa hawa Watendaji, walipwe kila mwezi. Kwa hiyo, Mheshimiwa Mwigulu, Mheshimiwa Waziri, lazima utoe paper itakayowa- instruct hawa Wakurugenzi, hakuna kuwaruka, vinginevyo hawa watakopwa. Sheria ya posho huwezi uka-carry forward, kama hautamlipa ndani ya mwaka wa fedha hautasema hili ni deni. Kwa hiyo, Wakurugenzi wengi wanaweza wakatumia kigezo hiki kutokuwalipa posho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu uamuzi wa kuwalipa Makatibu Tarafa ni wazo la busara sana. Hawa ndiyo viungo muhimu, wanafanya kazi kubwa katika Tarafa zetu kwa kweli, mmewapa vitendeakazi kwa maana ya pikipiki, posho hizi zitawasaidia kwenye mafuta, hongereni sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili naomba nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kuangalia suala la TARURA. TARURA tulizungumza hapa ndani ya Bunge kwamba, wanapata fedha ndogo, tumewaongezea fedha, jambo hili ni heri kabisa. Rai yangu Mheshimiwa Waziri, kuna Sheria ya TARURA ya mwaka 2007, Sheria ya Barabara, inakataza malori yenye zaidi ya tani 10 kwenda vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kijijini kwetu ndiko ambako kuna mazao, wafanyabiashara, hasa kipindi hiki cha mazao mfano kwangu mimi, huu ni msimu wa ufuta halafu utakuja msimu wa korosho, hakuna lori la tani 10 ambalo litatakiwa lipite. Kwa hiyo, nawaomba sana Mheshimiwa kwa kuwa tunaongezewa fedha naomba Mheshimiwa Waziri ije sheria tuibadilishe, hakuna lori la tani 10 kijijini kwetu malori yote ni kuanzia tani 15, tani 30.

Sasa leo unaposema tani 10 yasionekane vijijini maana yake yakae barabara kuu halafu gharama ya kuanza kutoa mazao kutoka vijijini kuleta barabara kuu, tunaongeza gharama ya uendeshaji. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakuomba sana hili mliangalie. Hii kero kubwa sana huko vijijini wananchi wetu wanalia, wafanyabiashara wanalia kwa sababu ya sheria hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni Property Tax. Imezungumzwa vizuri, Mheshimiwa Mwigulu nakuunga mkono kwa uamuzi wa kubadilisha njia ya ukusanyaji. Ni kweli 2017/ 2018 Property Tax ilikuwa inakusanywa na Halmashauri kabla ya 2017/2018 ikawa matatizo makubwa. Badaye Serikali Kuu kupitia TRA na sasahivi mmebadilisha utaratibu huu wa ukusanyaji, mimi nauunga mkono. Rai yangu kwao, kupitia LUKU katika wilaya zetu nataka kujua mgawanyo wa mapato utakuwaje? Najua watu watalipa Property Tax kutoka sehemu mbalimbali za nchi hii.

Je, ile Property Tax itakayokusanywa ndani ya wilaya yangu, itabaki ndani ya wilaya yangu au ndio ile asilimia 15 uliyoizungumza kwa utaratibu upi? Lazima tujue mgawanyo halisi wa Property Tax kwenye halmashauri zetu ili halmashauri zetu ziweze kufanya kazi inayostahili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Chumi amezungumza, kuna ahadi za viongozi. Viongozi wetu wanatoa ahadi nzuri sana, Mheshimiwa Mwigulu tunakuomba sana hizi ahadi za viongozi muwe mnaratibu na mnaziingiza kwenye bajeti. Isiwe jukumu la sisi Wabunge kuanza kufanya lobbing, kuanza kuwabembeleza kuna ahadi, kuna ahadi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi Mheshimiwa Rais alipokuja kwangu wakati wa kampeni aliahidi kujenga barabara ya lami kutoka jimboni kwangu kwenda Mkoa wa Morogoro kupitia Selous, ipo ndani ya ilani, lakini kwenye bajeti haipo. Lini itaingizwa ndani ya bajeti? Nilitarajia leo kingekuja kitabu hapa kikaeleza hizi ni ilani za viongozi wetu. Ilani hii itatekelezwa mwaka huu, ilani hii itatekelezwa mwaka huu, badala ya sisi kuanza kuja kuanza kubembeleza kuna ahadi! Waziri Mkuu 2018 aliahidi barabara kilometa tano ndani ya Jimbo langu, haipo popote tangu 2018 mpaka leo. Kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Mwigulu, tunaomba hizi ahadi za viongozi wetu mziratibu na mziingize ndani ya utaratibu wa bajeti ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Bajeti ya Serikali Mheshimiwa Mwigulu aliongelea mambo ya msingi mengi, mambo ya kupunguza tozo kwa ajili ya kuwasaidia wakulima wetu. Mimi naunga mkono mia kwa mia.

Rai yangu Mheshimiwa Waziri yale yote ambayo mmeyaeleza yatekelezwe ndani ya mwaka ujao wa fedha ili tutakapokutana tuweze kuisifia bajeti na utekelezaji wake, vinginevyo tutakuwa tunadanganyana. Naomba sana itekelezwe kama tutakavyokubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehrma ambaye ameniwezesha leo hii kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu kuchangia hotuba ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Pia naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana na kumpongeza Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya ya kuhakikisha kwamba nchi yetu inasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, nampongeza sana Waziri Mkuu na watendaji wote wa Ofisi yake ambao wameshiriki kwa njia moja au nyingine kufanikisha bajeti hii. Naomba nijielekeze katika Kilimo. Mimi natoka Jimbo la Nanyumbu. Ndani ya Jimbo langu, Korosho ndiyo uti wa mgongo wa wananchi wa Jimbo langu. Karibu asilimia 95 ya wananchi wanategemea zao hili la Korosho, hivyo naomba nichukue nafasi hii kumpongeza sana Waziri mwenye dhamana na Kilimo kwa kazi nzuri anayoifanya kuhakikisha kwamba zao hili la Korosho linasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2021 sisi ni mashahidi, Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi inayoongozwa na mama yetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ilitoa pembejeo bure kwa wananchi wote wanaolima zao la Korosho. Wananchi wa Jimbo langu walinufaika sana, kwa hili nashukuru sana. (Makofi)

Mheshmiwa Naibu Spika, kama hiyo haitoshi, mwaka huu Waziri mwenye dhamana ametangaza kwamba wananchi wote watakaolima Korosho ndani ya Jimbo la Nanyumbu watapata pembejeo bure kama ilivyo mwaka 2021. Hongera sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili naipongeza sana Serikali kwa kuhakikisha kwamba Maafisa Ugani walioko ndani ya wilaya yetu wanapewa vitendea kazi. Sisi ni mashahidi, karibu pikipiki 7000 zimetolewa na naamini kabisa lengo ni kuhakikisha kwamba kilimo kinasonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, tumeona Serikali imeongeza mitaji katika Benki ya Kilimo, Benki ya Kilimo iliyoanzishwa mwaka 2012 ilikuwa na mtaji na bilioni 60, Serikali imeongeza karibu bilioni 208, lakini Mfuko ule wa Ufaransa wa Maendeleo umeongeza karibu bilioni 210. Kwa hiyo kuna fedha nyingi ndani ya benki hii ambazo zina lengo kubwa la kuhakikisha kilimo chetu kinasonga mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mafanikio haya naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye korosho ili tuweze kuzalisha zaidi sio suala la pembejeo na viatilifu peke yake, kwa sababu ili korosho uweze kuvuna unahitaji kupalilia korosho. Katika hali ya kawaida, mkulima wa kawaida, hana uwezo wa kupalilia hekari 10 yeye mwenyewe kwa hiyo lazima ataajiri vibarua.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika korosho ili uweze kupata tija kupata mavuno mazuri, lazima upulizie korosho, unahitaji mabomba ya kupulizia, mafuta ya petroli, vibarua wa kukusaidia kupulizia, kwa sababu korosho una amka kati ya saa 8 usiku na saa 10 alfajiri kwenda kupulizia korosho, kwa hiyo lazima uajiri watu wa kukusaidia kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile ili upate mavuno mazuri lazima uwe na vibarua wa kuokota korosho zako, debe moja la korosho tunaokota kwa sh.1,500, lakini pia korosho unahitaji watu wa kukusaidia kuhamisha kutoka shambani na kupeleka nyumbani.

Kwa hiyo vitu vyote hivi vinahitaji fedha. Sasa Mheshimiwa Waziri ameeleza hapa kwamba kuna benki ambayo ya kumsaidia mkulima, naomba nitoe ushauri, wakulima hawa wapewe mikopo haraka iwezekanavyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, bila kuwapa mikopo hii pembejeo na viatilifu itakuwa kazi bure kwa sababu mikorosho itakuwa porini watashindwa kupalilia, watashindwa kupulizia, watashindwa kuokota, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri ahakikishe benki zetu CRDB, NMB, zinatoa mikopo kwa wakulima ili waweze kuzalisha kwa wingi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana kwa utaratibu huu huu wananchi walizalisha na Mheshimiwa Waziri ni shahidi, zaidi ya tani 26,000 zilizoongezeka, lakini bei ya korosho ilikuwa ndogo kuliko miaka yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha aeleze ni mambo gani yaliyosababisha bei ya korosho kuteremka na je, wananchi wanaambiwaje kuhakikisha kwamba msimu ujao bei itakuwa nzuri. Mambo haya tusipoyafanya tunaweza kuwavunja nguvu wakulima wetu, kwa hiyo namwomba sana Mheshimiwa Waziri aliangalie jambo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu, hili ni jambo ndani ya wilaya yangu. Namshukuru sana Mheshimiwa Waziri aliliingilia kati lakini bado halina ufanisi. Msimu umefungwa wakulima wa jimbo langu bado wanaidai Serikali, bado wanavidai vyama vya MAMCU zaidi ya sh.26,000,000, korosho wameuza, wamepeleka mnadani, mnada umefanyika, lakini wakulima bado hawajalipwa fedha zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri ametoa agizo kwamba walipwe ndani ya wiki moja. Nashukuru tutafuatilia kwa pamoja kuhakikisha wakulima wale wanalipwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ahadi ya viongozi wakuu; viongozi hawa wetu wanapokuja katika majimbo yetu wanatoa ahadi. Naomba sana ahadi hizi ziwe documented lakini zitekelezwa kwa muda husika. Nina ahadi kule tangu ya Awamu ya Pili ya Mzee Mwinyi mpaka leo haijatekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, ndani ya Kijiiji cha Mikuva Mheshimiwa Rais Ali Hassan Mwinyi aliahidi kujenga Kituo cha Afya mpaka leo haijatekelezwa, Waziri Mkuu 2018 aliahidi kujenga barabara za lami kilometa tano ndani ya jimbo langu, mpaka leo haijatekelezwa. Mama yetu Samia Suluhu Hassan wakati anainadi Ilani ya Chama Cha Mapinduzi aliahidi kutengeza barabara ya lami kutoka jimboni kwangu kupitia Selous hadi Morogoro mpaka leo haijatekelezwa na sijui itatekelezwa lini. Kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja aeleze hizi ahadi za viongozi zitatekelezwa lini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tatu ni kuhusu maji; maji ni uhai na ndani ya jimbo langu Mradi wa Maji kutoka Mto Ruvuma kuja Mji wa Mangaka ndio uliopo ndani ya Ilani ya Chama Cha Mapinduzi. Mheshimiwa Waziri alipokuwa anajibu hoja asubuhi alisema alisema hivi karibuni, sisi wananchi wa Jimbo la Nanyumbu tunataka kujua lini mradi huu wa maji wa Miji 28 utaanza kutelezwa lini tupate time, kwa sababu ukimpa mtu muda unampa matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka jana tumenunua ndoo shilingi 2,500, mwananchi wa kijijini anapata wapi uwezo wa kuzalisha hiyo hela akanunua maji. Kwa hiyo naishauri sana Serikali, mradi huu ni mzuri na wa maana sana tuambiwe lini mradi huu utaanza ili wananchi wangu waweze kuwa na imani na Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho ni la mawasiliano, tumeelezwa hapa Mkongo wa Taifa umeshafika Mtambaswala na umeunganishwa na Msumbiji, lakini nataka nikwambie kuna mambo ya ajabu sana ndani ya mkongo ule. Tulielezwa Mkongo wa Taifa faida zake kwamba, gharama za kupiga simu zitapungua, sidhani kama zimepungua. Tulielezwa mawasiliano yatakuwepo, mawasiliano mpaka sasa ni magumu, lakini pale Mtambaswala…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja naomba Serikali itekeleze hayo yaliyoelekezwa. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Spika, nami naomba kuchukua nafasi hii kwanza kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha siku ya leo kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu. Pili, naomba nimshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya ya kuhakikisha kwamba, Taifa letu linakwenda mbele. Tatu, naomba nimshukuru sana Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri sana ambayo jana amelielezea Taifa letu, hotuba ambayo ime-cover mambo mengi.

Mheshimiwa Spika, sasa kwa ufupi, naomba nizungumzie mambo mawili makuu ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameyazungumza katika hotuba yake. Mheshimiwa Waziri Mkuu amezungumzia suala la maji. Sisi sote tunajua changamoto zilizopo sasa hivi juu ya mabadiliko ya hali ya hewa, lakini namshukuru sana Waziri Mkuu, naishukuru sana Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi kwa jitihada ilizofanya kukabiliana na tatizo hili la maji, hasa katika Jimbo langu la Nanyumbu. Ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu wakati mama yetu Samia Suluhu Hassan anachukua nchi tulikuwa na changamoto kubwa sana ya maji. Ndoo ya maji ilifikia shilingi 2,500 ndani ya miaka hii miwili amefanya mapinduzi makubwa na sichelewi kuyaeleza ndani ya Bunge lako nini kimefanyika ndani ya jimbo langu.

Mheshimiwa Spika, wakati mama anaingia madarakani kata zifuatazo zilikuwa hazina maji kabisa na wala walikuwa hawajui nini maana ya maji ya bomba, lakini leo ninavyozungumza tuna maji ya bomba na wananchi wananufaika na huduma hiyo. Kata ya Nandete walikuwa hawajui kabisa huduma ya maji, Kata ya Mikangaula walikuwa hawajuikabisa huduma ya maji, Kata ya Nangomba, Kata ya Mikangaula Nangomba walikuwa hawajui kabisa, Kata ya Kamundi walikuwa hawajui kabisa, lakini ndani ya miaka miwili yamefanyika mapinduzi makubwa, leo wananchi wanajua nini maana ya mabomba na nini maana ya maji safi na salama. Jambo hili namshukuru sana Waziri Mkuu kwa kuisimamia Serikali vizuri na hatimaye wananchi wananufaika na huduma hizi.

Mheshimiwa Spika, ndani ya hotuba yake Waziri Mkuu amezungumzia upatikanaji wa maji katika ile miji 28. Wilaya yangu ya Nanyumbu ni moja ya wanufaika wakuu wa ile miji 28.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka kwamba, mwaka jana tulitia saini ule mkataba. Ule mkataba tulitia saini pale Ikulu kwamba, wakandarasi wale waje katika majimbo yetu na watekeleze mradi huu, lakini mradi huu umechelewa sana, ndani ya mwaka mmoja mradi haujaanza.

Mheshimiwa Spika, nimefurahi, jana mara baada ya Waziri Mkuu kuzungumza nikakutana na Waziri wa Maji na amenihakikishia kwamba, sasa kila kitu kimekamilika na huu mradi unakwenda kuanza. Naomba niwahakikishie wananchi wangu wa Jimbo la Nanyumbu, mradi huu unakuja kuanza na vijiji takribani 20 vitanufaika na mradi huu, hili ni jambo la kupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mradi huu wa maji pamoja na kwamba, unapita katika vijiji mbalimbali hadi kufika katika Mji wa Mangaka hapa ndipo kwenye walengwa wakubwa katika mji huu. Wananchi wa Mangaka wanashindwa kuwekeza katika miradi mbalimbali ya kiuchumi kwa sababu ya ukosefu wa maji. Leo utashangaa guest house zetu zote za Mangaka tunachukua maji ya kopo, hatuna maji ya bomba. Kwa hiyo, tuna imani kabisa kwamba, mradi huu utawezesha wananchi ambao wanaenda kuwekeza mbali na Wilaya yetu watarudi na kujenga nyumba nzuri, hoteli na hatimaye wale watu watalii wanaotoka Msumbiji kuja katika Mkoa wetu wa Mtwara watakuwa na mahali pazuri pa kufanya shughuli zao za starehe.

Mheshimiwa Spika, naomba pia niipongeze Serikali katika miradi, kuna miradi mikubwa ya mabwawa ndani ya jimbo langu. Kuna ukarabati mkubwa wa bwawa ndani ya Kata ya Sengenya ambao Serikali imetoa bilioni tatu na milioni mia nne, mradi huu unaanza hivi karibuni na takribani vijiji 10 vitanufaika na mradi huu; Mradi wa Upanuzi wa Bwawa la Sengenya.

Mheshimiwa Spika, katika Kata ya Maratani Serikali imejenga bwawa kubwa lenye thamani ya shilingi bilioni moja na milioni mia tano, lakini imeleta bilioni tatu na milioni mia sita kwa ajili ya kuweka mtandao wa mabomba, vijiji vinne vitanufaika na mradi huu, Kijiji cha Lipupu, Maratani, Mchanganee na Malema. Mambo yote haya ya maendeleo yamefanywa ndani ya kipindi kifupi chini ya utawala wa mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kweli, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama hiyo haitoshi, mradi wa uchimbaji wa visima. Ndani ya miaka miwili visima visivyopungua 25 vimechimbwa ndani ya jimbo langu na mikakati inaendelea katika kuhakikisha kwamba, sasa visima hivi vinawekwa mitandao ya maji, ili wananchi wanufaike.

Mheshimiwa Spika, baada ya kutoka hapo naomba niende kwenye mtandao wa barabara. Naipongeza sana Serikali, wakati mama yetu anaingia madarakani Jimbo langu la Nanyumbu lilikuwa linapata shilingi milioni 550 kwenye TARURA, leo ninavyozungumza tunapata bilioni mbili na milioni mia nne, ni jambo la kupongeza sana, lakini sio kupata fedha tu, fedha zile tunazisimamia. Mimi kama Mbunge wa Jimbo lile nahakikisha matumizi sahihi ya fedha, value for money, ionekane. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya miaka miwili tumeweza kujenga barabara kilometa 4.5 za lami, jambo ambalo ndani ya Wilaya ya Nanyumbu kitu lami kilikuwa hakipo ndani ya mji wetu. Leo ndani ya jimbo langu tumeweza kuweka taa za barabarani, jambo ambalo wananchi walikuwa hawajui kama kuna taa za barabarani. Hii yote imefanyika chini ya miaka miwili ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, ni jambo la kupongeza sana sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, tumeweza kujenga madaraja yasiyopungua 15, makalavati na vivuko mbalimbali, hii yote ni kwa sababu fedha zimekuja lakini tunazisimamia. Nami naomba niwape rai ndugu zangu Wabunge, fedha hizi zinapokuja tuwe wasimamizi wakuu wa hizi fedha. Tunatambua kwamba kuna TARURA, kuna Engineer TARURA lakini bado Mbunge una sababu ya kusimamia matumizi sahihi ya fedha hizi.

Mheshimiwa Spika, jambo la Tatu naomba niipongeze tena Serikali kwenye kilimo. Wilaya yangu ilikumbwa sana na baa la njaa. Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi chini ya Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan tuliomba msaada wa chakula cha bei nafuu na Serikali imetupatia takribani tani 1000. Wananchi wamepata mahindi ambayo yameuzwa kwa bei nafuu. Kuna baadhi ya watendaji ambao hawakuwa waaminifu walitumia fursa hii kujinufaisha.

Mheshimiwa Spika, ninampongeza sana Mkuu wetu wa Wilaya Mama Chaurembo na Kamati yake yote ya Ulinzi na Usalama kwa kazi kubwa waliyoifanya ya kupambana na hawa watumishi ambao siyo waaminifu na hivi ninapozungumza wengi wamepelekwa Mahakamani ili sheria ichukue mkondo wake. Kwa hiyo, mimi naipongeza sana Serikali ila rai yangu kwa Serikali, tunatambua tuna njaa, tunahitaji wananchi wawezeshwe pembejeo kwa wakati, mbolea kwa wakati ili waweze kuepukana na baa hili la njaa.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi kinachofanyika, mbolea iko mbali na wananchi, haiwezekani Wilaya ya Nanyumbu mtu afuate mbolea kilometa 54 toka alipo, hili jambo litakwamisha sana maendeleo ya wakulima wetu. Kwa hiyo, naomba sana Serikali iliangalie hili chini ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, mwisho naomba tena kuchukua nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa yale yote ambayo inaendelea kuyafanya ya kuhakikisha kwamba wananchi wa nchi hii wanaishi katika maisha bora na salama.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kupata nafasi hii. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Kilimo
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha mchana huu kusimama ndani ya Bunge lako hili Tukufu ili kujadilia bajeti hii ya Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitatoa shukrani kwa hawa wafuatao. Naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya wizara hii, Naibu wake, Katibu Mkuu, Mrajisi wa Vyama vya Ushirika na watumishi wote wa Wizara ya Kilimo ambao kwa njia moja au nyingine wameshiriki katika maandalizi ya bajeti hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi natoka Jimbo la Nanyumbu, jimbo ambalo ndilo ambalo linazalisha sana korosho, tunazalisha sana ufuta na tumeanza kujikita katika kilimo cha alizeti. Sasa kwa leo naomba nijielekeze kilimo cha korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitamshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama yetu Samia Suluhu Hassan ambaye kwa miaka miwili mfululizo ameweza kutupatia pembejeo bure. Hili jambo kwakweli nila kushukuru sana, kwa sababu moja ya changamoto ya wakulima ni upatikanaji wa pembejeo; lakini si pembejeo bure kwa mara ya kwanza pembejeo zimefika kwa wakati ndani ya wilaya yetu. Hili ninampongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tarehe 17 mwezi wa tano, Mkuu wetu wa Mkoa, ndugu yangu Kaguti amekuwa akishikiri katika kuhakikisha pembejeo zinasambazwa kwenda katika wilaya zetu. Kwa hiyo, mimi natoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Waziri na uongozi mzima wa mkoa kwa jitihada wanazofanya katika kuhakikisha kwamba kilimo chetu cha korosho kinakwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimewahi kuzungumza ndani ya Bunge lako kwamba pembejeo peke yake haitoshi, wananchi wetu wanahitaji fedha kwaajili ya palizi, kupulizia mikorosho, kuokota korosho na hatimaye kukusanya hizo korosho na kuzirudisha nyumbani. Lakini, wananchi hawana fedha. Kwa hiyo, tunatarajia benki zetu zi-support nguvu za wananchi, na nguvu za mama yetu. Hata hivyo, benki zetu zinatuangusha. Tarehe 28 mwezi wa nne MAMCU walifanya Mkutano Mkuu pale Masasi na Benki zote zilikuja pale, Mkuu wa Mkoa aliwaita akawahimiza kutoa mikopo kwa vyama vya msingi. Mimi nina vyama 37, lakini mpaka nianvyozungumza hakuna hata chama kimoja kimepata mkopo kwaajili ya zao la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tunakata kuinua zao la korosho, tutainuaje zao la korosho kama hatuwapatii mikopo wakulima wetu? Juzi hapa nimemsikia Mheshimiwa Waziri, ndugu yangu Mkenda, anasema Benki ya NMB imetoa bilioni mbili kwaajili ya mikopo kwa vijana wetu. Sasa, sasa hizi benki zinashindwaje kutoa mikopo kwa wakulima ili waweze kuinua zao letu la korosho? Kwa hiyo, ninakuomba sana kesho Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa anieleze na anishawishi; ni jitihada gani amezichukua kuzishawishi hizi benki ili ziweze kuwakopesha wakulima wetu; vinginevyo tunatwanga maji kwenye kinu. Hatuwezi kuinua zao la korosho kwa kutumia nguvu ya mwananchi kupata msaada kutoka kwenye benki zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu uadilifu kwa wataalamu wetu, hasa wafanyakazi wa ushirika. Tunawafanyakazi ambao si waadilifu, Ndani ya Jimbo langu msimu huu uliopita zaidi ya shilingi milioni 60 hazikuweza kulipwa kwa wakulima na chanzo kikubwa ni watumishi wa Idara ile ya Ushirika. Jambo hili Mheshimiwa Waziri analifahamu sana, kwamba tunao watumishi pale si ambao si waadilifu lakini wanaachiwa. Tunakuja kuwaeleza jamani huyu mtumishi si mwadilifu lakini wanasema huyu ndiye anafanya kazi. Sasa, kama anafanya kazi basi mumchukue nyinyi kwa sababu kule kwa wananchi amesababisha matatizo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hakuna kitu ambacho kinaudhi kama mkulima amelima korosho, amepeleka godown halafu asipate fedha. Halafu mfanyakazi wa ushirika ambaye ndiye Internal Auditor katika AMCOS anasema kwamba AMCOS zote hazina matatizo, lakini kumbe kuna matatizo kibao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi ninamuomba sana Mheshimiwa Waziri, hawa watumishi ambao tunakuja kukuletea malalamiko uchukue hatua immediately. Haiwezekani wakulima wanapata tabu, na tukienda sisi Wabunge tunalalamikiwa kama vile sisi ndio tumesababisha matatizo hayo kumbe ni watumishi wenu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine ninayoiona kwa hawa wafanyakazi wa ushirika wanawatu wawili wanaowajibika kwao kuna Mkurugenzi wa Halmashauri halafu kuna Mrajisi wa Vyama. Sasa naomba sana Serikali iamue hawa watumishi wapelekwe eneo moja. Na mimi ningeomba hawa watumishi wa ushirika wote waende kwa Mrajisi ili waweze kuwajibika moja kwa moja; vinginevyo wale watumishi kule wanakuwa kama miungu watu. Wao badala ya kuvisimamia hizi AMCOS wao ndiyo wanakuwa wenye AMCOS. Wananchi ambao ndio wenye AMCOS wanaweka pembeni wao ndio wanakuwa miungu watu. Sasa hili jambo kweli halikubaliki, hatukubali kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kesho Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa aeleze ni jitihada gani amezifanya kwa hawa watumishi ambao wamesababisha hasara kubwa ndani ya wilaya yangu, wamesababisha kadhia kubwa ndani ya wilaya yangu na bado wapo ndani ya wilaya yangu. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naomba kuunga mkono hoja, nategemea majibu mazuri sana kutoka kwa Mheshimiwa Waziri kesho. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii kutoa mchango wangu juu ya hotuba hii ya bajeti ya kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema ambae ameniwezesha jioni ya leo kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nichukue nafasi hii kuwapongeza sana wakulima wa Jimbo langu la Nanyumbu. Natambua changamoto kubwa ambazo wanakumbana nazo katika kuhakikisha kwamba kilimo hasa kilimo cha korosho kinakwenda mbele. Kwa hiyo naomba nichukue nafasi hii kumjulisha Mheshimiwa Waziri changamoto ambazo wakulima wangu wa Jimbo la Nanyumbu wanakumbana nazo katika kuhakikisha kwamba kilimo chetu cha korosho kinakwenda mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika mwaka huu uliokwisha kilimo cha korosho ndani ya taifa letu kimeshuka sana, kutoka tani 240,000 hadi tani 182,000. Hii yote kulingana na maelezo ya Mheshimiwa Waziri ni kwamba imesababishwa na hali ya hewa. Lakini naomba nichukue nafasi hii kulijulisha Bunge lako Tukufu pamoja na kwamba kilimo cha korosho kimeshuka lakini ndani ya Wilaya yangu ya Nanyumbu kilimo cha korosho kimepanda katika uzalishaji wake. Kwa hiyo basi nachukua nafasi hii kuwashukuru sana na kuwapongeza wananchi wangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini wananchi wangu wanavyo changamoto zifuatazo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ni bei isiyoeleweka ya korosho. Jambo hili ni changamoto kubwa sana kwa wakulima wetu. Nimewahi kushauri ndani ya Bunge lako, kwamba kwa nini Serikali yetu, kwa nini Wizara isitoe bei elekezi ya zao la korosho ili mkulima akajipanga na akajua kwamba gharama zangu za uendeshaji ni shilingi ngapi na nitapata faida kiasi gani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakulima wetu wanakwenda kama maisha ya kubahatisha, hawajui mwaka huu bei ya korosho itakuwa kiasi gani; na hii inadhorotesha uzalishaji wa bei ya korosho. Kwa hiyo namuomba sana Mheshimiwa Bashe ajaribu kuliangalia jambo hili, atoe bei dira, bei ambayo itawawezesha hata wanunuzi wanaokuja kuanza kuanzia katika eneo lile. Kukiwa na bei dira wale wanunuzi uchwara wanunuzi wadogowadogo hawatakuja katika mnada, watawaacha wanunuzi ambao wako serious na kuhakikisha kwamba bei ya mkulima inakuwa nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine, wakulima wetu, hasa wa korosho, wana changamoto na mikopo, benki zetu haziwasaidii wakulima wetu. Jambo hili nimelizungumzia sana, na Mheshimiwa Bashe analifahamu. Kwa wale wasiojua korosho, korosho si pembejeo tu. Niishukuru sana Serikali imetoa pembejeo kwa wakulima, jambo hili mimi nalipongeza sana. Lakini kumpa tu pembejeo hakusaidii, korosho unahitaji kupalilia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtu mwenye ekari kumi ana mikorosho 240 huwezi ukapalilia wewe na mkeo, ni lazima utahitaji vibarua, na ndiyo maana tunakwenda kwenye taasisi za benki kuomba mkopo ili fedha zile tutumie kwenye kupalilia mikorosho. Tunahitaji mikopo ili kuweza kununua mafuta na kuweza kupulizia mikorosho; na mikorosho huwezi ukaipulizia peke yako, hekari kumi unahitaji kuwa na watu wa kuwakodisha ili wakusaidie kupulizia. Tunahitaji vibarua wa kuokota korosho, ndoo moja tunaokota kwa shilingi 2000, ukiwa na mikorosho 2400 huwezi ukaokota wewe na mkeo inahitaji vibarua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana tunaomba taasisi za benki ziwakopeshe hawa wananchi ili waweze kutumia mikopo hiyo katika uzalishaji na kuinua pato la taifa. Sasa ndugu yangu Bashe Waziri msikivu, jambo hili la mikopo benki zetu wanashindwa vipi kuwapatia wakulima wetu? Leo ni mwezi wa tano, mwezi wa sita maandalizi ya zao la korosho yanaanza huku benki ikiwa bado hawatoi mikopo kwa wananchi wananchi wanahangaika kule. Kwa hiyo namuomba Mheshimiwa Bashe hili jambo aliangalie sana katika mstakabali mzima wa kuinua zao letu la korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwenye bajeti yake Mheshimiwa Bashe amazungumza suala zima la umwagiliaji, mimi nampongeza sana. Hata hivyo nina masikitiko makubwa. Sisi tumepitiwa na Mto Ruvuma. Mto Ruvuma ukianzia Mtwara Vijijini kwa Bwana Chikota kule hadi jimboni kwangu mpaka Tunduru; mimi ndani ya jimbo langu nimepata mradi mmoja tu wa kuchimba bwawa katika Mto Ruvuma, hili jambo linasikitisha sana. Tuna maeneo makubwa ya umwagiliaji kuna watu wamezungumza hapa, naishukuru Serikali kwa kuapta miradi ya skimu ya umwagiliaji miradi 11 miradi 15 mimi mradi mmoja na sijui kama utafanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namuomba Mheshimiwa Bashe next time awe mwangalifu na miradi ya namna hii. Haiwezekani sehemu moja inapata mradi mmoja wengine wanapata miradi kumi, kumi na tano, hili jambo si sawa. Wote tunatambua mabadiliko ya hali ya hewa, jambo hili linaathiri nchi nzima, na suluhisho la mabadiliko ya hali ya hewa ni kwenda kwenye kilimo cha umwagiliaji. Sasa inakuwaje leo katika eneo kama lile ambalo ndio wazalishaji wakubwa unatoa mradi mmoja wa bwawa? Hili jambo si sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namuomba sana Mheshimiwa Bashe hili jambo aliangalie ili tutakapokuja mwakani tuhakikishe miradi hiyo ya umwagiliaji inakwenda sambamba nchi nzima. Hata hivyo naishukuru sana Serikali tunao mradi mmoja wa uchimbaji bwawa ukachimbwe bwawa. Tutatarajia mwakani tuje hapa tujue lile bwawa ambalo lilienda kuchimbwa katika Kata ya Masuguru likachimbwe ili wasaidie shughuli za umwagiliaji kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba kuchangia kuhusu suala zima la bei ya pembejeo, mbolea. Ndani ya wilaya yangu pembejeo, hasa mbolea, mwaka huu haikuwepo. Muuzaji wa pembejeo alikuwa napatikana kilimeta 54 kutoka wilayani. Jambo hili kwa kweli lilinihuzunisha sana, na niliwasiliana na Mheshimiwa Waziri, na Mheshimiwa Waziri akaahidi kwamba atafanya mabadiliko. Lakini naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri, kwa nini tusivitumie vyama vyetu vya msingi kuwa mawakala wa kuuza pembejeo hizi? Kwa sababu vyama vyetu vya msingi kule kwetu wako karibu kila kata, kwa hiyo mbolea hii itakuwa rahisi kuigawa na kuisimamia marejesho yake kama itahitajika kurejeshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumza hivyo kwa sababu wakulima haiwezekani akasafiri kilometa 54 kwenda kuifuata mifuko miwili kule halafu akarudi kilmeta 54, ni mbali sana. Kwa hiyo kama mbolea inakuwa ni shilingi 70,000 haitakuwa tena 70,000, itafika 90,000 mpaka 100,000; kwa hiyo itakuwa haujamsaidia mkulima. Ninaomba sana Serikali kwa hili la pembejeo nalo litiliwe mkazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine naomba pia kuzungumzia masuala ya ujenzi wa mabwawa, nimezungumza kwamba tumepangiwa bwawa moja pale Masuguru, lakini sisi katika wilaya yetu tunayo mabwawa ambayo sasa hivi endapo yangeendelezwa yale yaliyopo yangesaidia sana kutatua kero hii. Mfano Nangomba mimi ninalo bwawa, pale Chipweputa kwenye Kijiji cha Lomasogo ninalo bwawa na sehemu nyinhine nazo kuna mabwawa. Yale mabwawa nilitegemea sasa yangekuja kuboreshwa ili yaweze kuinua suala zima la umwagiliaji

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la kuongeza thamani mazo yetu. Ninatambua kwamba Wizara ina mkakati mkubwa wa kujenga kiwanda kikubwa katika Mkoa wa Mtwara. Naomba nishauri, tunayo majengo katika Mkoa mzima wa Mtwara. Tunayo majengo maeneo ya Newala, Mtwara Mjini na Masasi. Sasa, kwa nini tusitumie majengo yale kuweka mashine ili kuweza kubangua korosho zetu badala ya kutumia nguvu nyingi….(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa muda wako umekwisha.

MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo machache naunga mkono hoja hii, nashukuru sana. Natambua kwamba mwakani Wizara itafanya mambo makubwa sana katika Wilaya yangu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii jioni ya leo ili nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi. Naomba nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha mimi jioni hii kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu kutoa mchango wangu kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kama ilivyo ada nami naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa yale yote ambayo ameyafanya katika Wizara hii. Sisi ni mashahidi hadi mwezi Mei Wizara hii imepata asilimia 82 ya makisio yake, lakini wote sisi ni mashahidi tumeona jinsi gani Mama Samia Suluhu Hassan alivyokuwa na uchungu na wananchi wake na kusamehe madeni yale ya nyuma ili wananchi waendelee kulipa katika muda unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, Mheshimiwa Rais ameweza kutafuta fedha nyingi karibu bilioni 345 na kuwakabidhi Wizara ya Ardhi ili Wizara hii iweze kutenda yale ambayo wananchi wanayatarajia. Ni matarajio yangu kuwa watendaji watazitumia fedha hizi vizuri sana ili wananchi waweze kuona matokeo ya fedha zao. Sina shaka kabisa na Mtendaji Mkuu wa Wizara ndugu yangu Sanga, uaminifu wake, uadilifu wake unajulikana huko alikotoka na nina imani ataitendea haki Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, namshukuru tena Mheshimiwa Rais kwa kuunda ile Kamati ya Mawaziri Nane wa Kisekta ambao wamezunguka Tanzania nzima kutafuta majawabu ya matatizo ya wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa naomba nijielekeze katika mchango wangu. Mheshimiwa Rais aliunda Wizara ya Kisekta ya Mawaziri Nane, Mawaziri hawa walitembea almost katika nchi yote hii na bahati nzuri katika Mkoa wa Mtwara walifika. Mheshimiwa Waziri yeye ni shahidi tulikuwa naye pale Mtwara na tulikutana nae. Yeye ni shahidi aliona jinsi gani watendaji wake walivyofanya kazi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jambo la kushangaza sana sisi Wabunge ambao ndio wawakilishi wa wananchi hatukushirikishwa kabisa katika mchakato huu. Ndani ya wilaya yangu, Kata ya Mkonona Vitongoji vya Wanika, Kitongoji cha Nambunda na Malomba. Vitongoji hivi vimehusika kabisa katika mchakato mzima wa kuhakikisha kwamba wananchi walipo ndani ya eneo hili wanahamishwa na kutafutiwa makazi katika eneo lingine. Cha kushangaza halmashauri kwa maana ya Madiwani sisi hatukushirikishwa hata siku moja. Kwa hiyo, kila kitu kilifanyika siri na Mheshimiwa Waziri mwenyewe ni shahidi na alishangaa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa Mtwara alipogundua jambo hili alitumia hekima kubwa na kulimaliza jambo hili kwa busara sana na tukashiriki kikamilifu, tukaondoka sisi, Wabunge na Kamati nzima ya Waziri mpaka katika eneo la tukio na aliona jinsi wananchi wasiopungua 10,000 wako pale ndani ya eneo wakisubiri maamuzi ya Serikali. Sasa Serikali imeshafanya maamuzi na sisi hatuna tatizo na maamuzi na Waziri ameikabidhi Serikali ya Mkoa iandae mchakato mzima. Najiuliza Serikali ya mkoa wanazo nyezo za kufanyia kazi maamuzi ya Waziri. Serikali ya Mkoa wamefanya tathmini ya wananchi wahame, wamewatafutia maeneo wananchi waende, lakini mpaka sasa hivi wananchi wale wanasubiri fidia ambayo ndani ya ripoti ya wataalam wamezungumza bayana kwamba wananchi wapewe fidia ili wahamie maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri, Wizara ifanye maamuzi sasa na sina uhakika kama ndani ya bajeti hii wale wananchi wa Wanika na Malomba, Nambunda wametengewa fedha ili waondoke katika maeneo hayo na waende katika yale maeneo ambayo wamepangiwa. Kama eneo hili halitashughulikiwa kesho nitatoa shilingi. Sitakubali wananchi wale waendelee kukaa miaka saba wakisubiri maamuzi ya Serikali, tunawatia umaskini wananchi wale. Kwa hiyo kesho Mheshimiwa Waziri atakapokuja hapa atueleze wananchi wale lini watalipwa fedha zao ili waende eneo ambalo Serikali ya Mkoa imeshawapangia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili ni suala la migogoro. Migogoro imekuwa karibu kila mahali katika nchi hii na ndani ya Wilaya yangu ya Nanyumbu migogoro ipo. Naishukuru sana Wizara katika hotuba yake Mheshimiwa Waziri ameeleza jinsi gani ya kuweza kupunguza migogoro na ni kweli ndani ya wilaya yangu mimi nina masikitiko makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ile hatuna Baraza la Ardhi la Wilaya, matatizo yetu yanakwenda kilometa 100 ups and down mwananchi anapopata matatizo ndani ya Wilaya ya Nanyumbu inabidi aende Masasi ambapo ndipo kuna Baraza la Ardhi, jambo hili linakwamisha utoaji wa haki kwa wananchi, jambo hili pia linasababisha wale wenye fedha ndiyo wanapata haki, kwa sababu mgogoro uko Nanyumbu, kesi iko kilometa 50, huyu mwananchi maskini ataweza kwenda kilometa 50?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri nakupongeza sana kwa kuamua kuunda Mabaraza ya Ardhi kwa kila Wilaya, wasiwasi wangu naomba kesho utakapokuja unithibitishie, Wilaya ya Nanyumbu Baraza la Ardhi litakuwepo katika mwaka ujao wa fedha? Vinginevyo kesho patakuwa matatizo makubwa Mheshimiwa Waziri, sitakubali tupite tena mwaka mwingine bila kuwa na Baraza la Ardhi la Wilaya ya Nanyumbu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasaema hivyo kwa sababu wananchi wanahangaika, leo unapigiwa Mbunge fedha umsaidie kwenda kwenye kesi Masasi, hili jambo siyo sawa hata kidogo. Kwa hiyo, lazima tuwasaidie wananchi wetu katika kutafuta haki vinginevyo watakuwa wanapata haki wale watu ambao wana fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda sana kulizungumzia hapa ni haya makampuni yanayopewa kazi kuja kufanya shughuli za upimaji katika maeneo yetu. Tunayo kampuni ambayo ilikuja kufanya upimaji wa ardhi katika maeneo yetu ili wananchi baadae wapate hati, ile kampuni mpaka leo imefanya ile kazi, wananchi hawajapata hati na wananchi wanahangaika. Jambo hili nilishalifikisha ndani ya Wizara na Wizara ikaahidi, tena kampuni yenyewe ni ya Serikali, Chuo cha Ardhi Morogoro lakini cha kushangaza mpaka leo wananchi wale wanahangaika, wananchi wale nikifika tu kutoka Dodoma wanajaa ofisini kwangu kuomba kujua ufafanuzi wa hatma yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nakuomba sana, naiomba sana Wizara haya ambayo Wabunge tunashauri wayafanyie kazi. Kampuni hii kama kweli ipo, basi ilete hati ambazo wananchi wale wamechanga fedha zao na wanahitaji sasa kupata hati ili mambo yao yaendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kuhusu hati za kimila; hati za kimila zinatolewa, Mheshimiwa Waziri amezungumza kwamba unaweza ukaitumia hati ya kimila kupata mikopo. Mimi naomba anithibitishie hili, kesho atakapokuja kuhitimisha anielezee tu wananchi japo wanne wa Wilaya ya Nanyumbu ambao wana hati za kimila, wamepata mikopo katika benki zetu, vinginevyo tutakuwa tunadanganyana, tuelezwe ukweli hati za kimila, dhamira yake ni nini? Ukipata hati ya kimila, unapata mkopo? Lakini siyo unanipa karatasi ambayo mimi haina manufaa yoyote, kwa hiyo naiomba sana Wizara kesho ituthibitishie hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naiunga mkono hoja, nashukuru sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipatia nafasi hii ili nami niwe mchangiaji katika bajeti hii ya Serikali. Awali ya yote naomba pia nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema ambaye ameniwezesha jioni ya leo kusimama mbele ya Bunge lako tukufu. Aidha, kama ilivyo ada nami naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kazi kubwa anayoifanya katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni mashahidi, kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ameeleza bayana kwamba pato la Taifa limeongezeka kutoka bilioni 68 hadi 85, jambo hili ni la kujivunia sana. Jambo hili linajidhihirisha kwenye huduma za jamii katika maeneo tunayotoka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi ni mashahidi, kwenye Jimbo langu la Nanyumbu, miradi mingi ya maendeleo imefanywa ndani ya miaka hii miwili na mwaka uliokwisha. Kuna miradi mikubwa ya maji; Mradi wa bilioni 3.6 kwenye Kata ya Maratani ambao kwa kweli ni mkombozi wa wananchi wa Jimbo langu. Kuna Mradi mkubwa wa bilioni 3.4 katika Kata ya Sengenya, lakini tuna mradi wa bilioni 40 wa kutoa maji katoka Mto Ruvuma kuleta katika Mji wa Mangaka. Miradi hii ya maji ilikuwa ni kero kwa wananchi na imekuja kukomboa wananchi wa jimbo langu. Namshukuru sana Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mama yetu ameonesha ukomavu, amerudisha demokrasia. Sisi ni mashahidi, leo hii Vyama vya siasa vimeruhusiwa kufanya siasa, jambo ambalo lililkuwa ni ndoto. Vile vile, amerudisha mchakato wa Katiba Mpya, kwa kweli jambo hili jambo hili linatia moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya miaka hii miwili tumeona kiwango cha investment kilichowekezwa ndani ya nchi yetu, zaidi ya trilioni 23, karibu nusu ya bajeti yetu imeingizwa katika uchumi wetu. Ni jambo la kumshukuru sana Mama amekuwa muungwana, wafadhili na wawekezaji wamekuja kuwekeza ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, tuliona zile fedha za Covid ambazo kwa busara ameweza kuzitumia katika kujenga shule na miradi ya maji. Ndani ya Jimbo langu nimenufaika na hizi fedha za Covid karibu madarasa 68 yalijengwa. Vile vile, mradi wa maji wa bilioni moja ulijengwa ndani ya Jimbo langu na kuondoa kero hii kubwa ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia pato la mtu mmoja mmoja (per capita income) imeongezeka kufikia dola 1,252. Kwa hiyo, kwa haya yote na mengine namshukuru sana Waziri wetu wa Fedha na Naibu wake kwa ushauri mzuri wanaoufanya kwa Mheshimiwa Rais ambayo haya yote leo tunayoyaona yanafanyika ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa nichangie kidogo kwenye bajeti hii. Tumeona makadirio yetu ya kodi katika mwaka ujao wa fedha ni karibu trilioni 44.3. Makadirio haya ya kodi yanatokana na vyanzo mbalimbali, kuna direct tax na indirect tax, kwa hiyo hizi kodi ili zikusanywe lazima tuwe na watumishi waadilifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba, kuna vyanzo vya kodi ambavyo kwenye ripoti ya CAG vilileta hoja nyingi sana, ningemwomba Mheshimiwa Waziri aangalie kama kuna uwezekano hebu tubadilishe jinsi ya kukusanya hizi kodi. Mfano, ukiangalia taarifa ya CAG hii kodi ya withholding tax imekuwa na hoja nyingi. Waajiri wanakusanya withholding tax at source lakini hawapeleki TRA. Sasa nini matokeo yake? Matokeo yake yule mtu aliyekatwa anapoenda kukadiriwa kule TRA inaonekana hajalipa chochote. Kwa hiyo, yule aliyekata ananufaika lakini yule aliyekatwa inakuwa ni tatizo kwake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kwamba, kwa nini tusitumie mabenki kukusanya hizi pesa na kuzipeleka TRA? Mwajiri alipe kama ilivyo deni la mhusika lakini benki ndiyo ikate hizi pesa na at the end of the day benki anapeleka TRA moja kwa moja na mtu anapotaka kujua amelipa kiasi gani anaenda kwenye website ya TRA ana-click button anapata kiasi alichochangia katika ile final payment analipa ile tofauti na jambo hili tutaondoa hata kero hoja za ukaguzi ambazo miaka na miaka tunakuwa tunakutana nazo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye direct tax nyingine ambayo tumekutana nayo ni tumekuwa waagizaji wakubwa wa magari kutoka nje ya nchi, lakini watu wengi wameshindwa kukomboa magari yao kutokana na kodi. Sasa wakati umefika tukubaliane, mtu anapoagiza magari nje ya nchi alipe na kodi moja kwa moja. Kama kodi inajulikana ni shilingi milioni tano gari milioni 30 alipe milioni 35 moja kwa moja. Hii itasaidia sana kupunguza hizi bonded warehouse ambazo zinahifadhi magari miaka kumi, miaka 15 mtu hana hela ya kulipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo itatusaidia sana, kwanza itarahisisha kukusanya kodi kwa mara moja lakini pili itapunguza mzigo kwa watumishi wa TRA. Watumishi wa TRA kazi yao itakuwa inakuja tu paper work kuangalia hii ndiyo gari uliyoagiza? Hii ndiyo CC number? Hii sijui na nini na nini, at the end of the day maisha yanakuwa mepesi. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo tutarahisisha sana na kukusanya hela kwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye indirect tax, hii pia ni kodi ambayo mwananchi anaweza akalipa bila kujihisi kwamba amelipa kodi, hiki ndiyo chanzo ambacho tukitumie zaidi na zaidi, sasa nilikuwa nimeangalia hapa hawa ETS wao wameingiza katika baadhi ya bidhaa ku-stamp bidhaa zetu, kwa ku-stamp imesaidia sana, kwanza inamtambulisha kwamba hii bidhaa ni ya Tanzania lakini pili inarahisisha kuondoa bidhaa feki, tatu inaweza kujua ni kiasi gani cha kodi ambacho kinaweza kukusanywa kwa mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo lazima tuwatumie hawa katika bidhaa mbalimbali, hebu tuongeze wigo wa bidhaa zetu. Mfano Mheshimiwa Waziri amezungumza kuongeza kodi kwenye vifaa vya ujenzi, badala ya kuongeza kodi hebu tuende kwa utaratibu huu tuone tuki-stamp hizi cement tunayozalisha je, hatuwezi kukusanya kodi nyingi kuliko kuongezea wananchi kodi. Kwa hiyo, nilikuwa nashauri katika maeneo hayo mawili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho naomba tena nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwa kweli Mheshimiwa Waziri wewe hujioni lakini umekuwa mtu laini sana, unafikika. Kulikuwa na Mawaziri hapa Waziri wa Fedha ananata huwezi kuamini kama huyu ni binadamu, lakini wewe tunakutana wewe Yanga mimi Simba tunachati unaondoka zako maisha yanaendelea, hii imerahisisha watu kukuambia mambo mengi ya msingi. Kwa hiyo, usiache tabia hiyo na wananchi wanakujua unafikika. Sasa kwa kuwa unafikika tunakuomba sasa urahisishe uwezekano wa wananchi kurahisisha maisha yao, kubali hoja zao zifanyie, kazi ndugu yangu Shabiby amesema hoja za wananchi zichukuliwe kama ni changamoto, zifanyiwe kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba tena nishukuru sana Serikali kwa miradi mbalimbali ambayo imeendelea kutekelezwa ndani ya Jimbo langu. Jimbo la Nanyumbu tulikuwa hatujawahi kuona barabara ya lami na taa za barabarani lakini ndani ya Mama Samia tumeyaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo baada ya kusema hayo najua muda siyo rafiki naunga mkono hoja mia kwa mia, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nichukue nafasi hii mchana huu kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri, Katibu Mkuu wa Wizara hii Ndugu yangu Sokoine na wafanyakazi wote wa Wizara ya Mambo ya Nchi za Nje ambao kwa njia moja au nyingine wameshiriki kikamilifu katika maandalizi ya bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nijielekeze katika maeneo matatu; kwanza juu ya diplomasia ya kiuchumi na hususan katika Mkoa wangu wa Mtwara ndani ya Jimbo langu la Nanyumbu. Pale ndani ya Jimbo la Nanyumbu tunalo Daraja la Umoja, daraja lile ndiyo kiungo kati ya Mkoa wa Mtwara na Msumbiji, ndani ya daraja lile Serikali yetu ya Tanzania imejenga barabara kwa kiwango cha lami hadi pale darajani. Sasa ukivuka lile daraja ndiyo unafika Mji unaoitwa Ngomano, ukivuka lile daraja na kutoka pale Ngomano unakwenda kilometa 300 unakutana na mji unaoitwa Silver Makua. Sasa pale ndiyo kuna njia panda ya kwenda Maputo na huku unakwenda mji mmoja unaitwa Pemba hadi Mtwara kwa upande ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kutoka pale Silver Makua kuja hapa Ngomano ni kilometa 300; bahati mbaya sana barabara ile mpaka leo ni ya vumbi. Lakini kulikuwa na makubaliano ya kimsingi kabisa kwamba Tanzania inajenga kwa kiwango cha lami hadi pale darajani na wale wenzetu upande wa pili wajenge kwa kiwango cha lami. Barabara hii ni muhimu sana katika kuifungua nchi yetu na hasa kwenda Msumbiji hadi South Africa, mfano mwezi Aprili pale Mtambaswala kituo chetu cha TRA kimekusanya shilingi 1,400,000,000; mwezi wa tatu shilingi 1,200,000,000; mwezi wa pili halikadhalika. Kwa hiyo, kuna mapato mengi ambayo Serikali yetu inakusanya kupitia pale.

Sasa rai yangu kwa Mheshimiwa Waziri naomba uendelee kufanya mazungumzo na Serikali ya Msumbiji, wafanye jitihada za makusudi kuweza kujenga barabara ile ya kiwango cha lami kutoka pale Silver Makua kuja pale Ngomano ni kilometa 300 tu kwa kufanya hivi ninaimani kabisa nchi yetu itafunguka na wananchi wetu watafanya biashara sana. Kwani hivi sasa hivi ninavyoongea mbao zote ngumu zinapita pale, hii shilingi bilioni 1.5 ni usafirishaji wa mbao, uingizaji wa magari, uingizaji wa mitambo na mambo mengine mengine. Kwa hiyo, kuna mambo mengi mazuri yakifanyika tutafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili unahusu masuala mazima ya ukusanyaji wa mapato ndani ya Wizara hii. Mheshimiwa Waziri alipokuwa anaeleza hapa ameeleza mapato mbalimbali ambayo Balozi zetu inakusanya kwamba moja ya chanzo kikubwa ni pango, lakini hata Kamati imeeleza vyanzo mbalimbali vya mapato kule Ubalozini na changamoto ambazo Balozi zinakumbana nazo.

Sasa Mheshimiwa Waziri naomba nikushauri; tunalo Shirika letu la Nyumba, Kamati imezungumza tutumie sekta binafsi, tutumie mashirika yetu ya Tanzania yaweze kufanya shughuli hizi. Kwa kusema Serikali ijenge nyumba sasa hivi una Balozi 45 hutaweza Mheshimiwa Waziri. Tunalo Shirika letu la Nyumba, tumefanyiwa semina hapa na Ndugu yetu Msechu tunauona uwezo wao wa lile shirika, kama tatizo ni sera ni suala la kubadilisha ili shirika nalo likawekeze nje ya nchi. (Makofi)

Kwa kufanya hivi Mheshimiwa Waziri utakuwa umefanya mambo matatu makubwa; kwanza utakuwa umeweza ku-save fedha za kigeni. Tunatumia fedha nyingi za kigeni kupeleka nje ya nchi kila mwezi kwa ajili ya kulipia nyumba za wafanyakazi na Ofisi za Kibalozi. Tukitumia Shirika letu la Nyumba fedha za kigeni hazitatumika badala yake tutaweza kutumia fedha zetu za Tanzania kuilipa National Housing.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine Balozi zetu tukijenga kule Ofisi mfano Paris, Mheshimiwa Waziri unaingiza milioni 400 mpaka 600 kwa mwaka kwa sababu Ubalozi wetu wa pale pia tumewapangisha baadhi ya Balozi. Halikadhalika tukitumia shirika letu hili litaweza kujenga nyumba, ofisi na kuweza kupangisha Balozi zingine.

Kwa hiyo, ni wakati muafaka sasa hivi Mheshimiwa Waziri uendelee kutumia shirika letu ili liweze kujenga nyumba zetu kwa kufanya hivyo utaokoa sana. Tumeona mwaka jana hapa miradi ya maendeleo umeshindwa kutumia hata senti tano kwa sababu hukupata fedha na Kamati imezungumza haikutumika hata senti moja kwa ajili ya miradi ya maendeleo. Mwaka huu umeomba shilingi bilioni nne ni hela ndogo sana, huwezi kujenga, una Balozi 45 na tunategemea kufungua Balozi zingine. Kwa hiyo, lazima tushirikishe sekta binafsi na mashirika yetu ambayo yanajihusisha na masuala ya ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni suala la watumishi; nimemsikiliza sana Waziri kwamba mwaka jana watumishi wengi walikwenda Balozini, hili jambo nimelipenda sana na utaratibu huu Mheshimiwa Waziri uendelee, kila baada ya miaka minne kama sera inavyosema watumishi wanaokwenda waende na wanaorudi warudi. Ila tunazo changamoto, wale wanaorudi mara nyingi hawabakishwi makao makuu, wanaondolewa na kupelekwa sehemu nyingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara hii ndugu zangu ni Wizara muhimu sana watumishi wake wawekwe katika eneo moja. Haiwezekani mtumishi umemtoa Ubalozini umem-train, ana knowledge kubwa ya Ubalozi unafika hapa unampeleka kwenye Halmashauri. Unaenda kumuanzisha upya, unapoteza resource kubwa ambayo umeiweka. Sasa lazima hawa watumishi wakifika hapa tusiwaone kama maadui, yaani kuna chuki fulani inajengwa kwamba huyu ameula, ameula nini yeye ni resource, lazima huyu tumlee, tumlee ili baada ya muda tumpeleke tena. Kwa hiyo, kwa kufanya hivyo mimi ninaimani kabisa hii diplomasia ya kiuchumi tunayoihubiri hapa itakwenda na itatekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. YAHYA A. MHATA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami naomba nichukue nafasi hii kuchangia huu Muswada wa ukusanyaji wa fedha au Finance Bill ambao uliwasilishwa na Mheshimiwa Waziri. Muswada huu ni mzuri na una lengo la kuisaidia Serikali kuweza kukusanya fedha ili yale ambayo tulikubaliana yaweze kutendeka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naipongeza sana Serikali, nampongeza sana Waziri mwenye dhamana na Wizara hii kwa kazi nzuri aliyoifanya kwenye bajeti ya mwaka huu na huu Muswada aliotuletea. Nina uhakika leo hii narudi ndani ya Jimbo langu nikiwa na uhakika wa vyanzo zaidi ya vitano vyenye fedha, zaidi ya shilingi bilioni tatu katika Jimbo langu. Nina uhakika wa kupata shilingi milioni 500, jambo ambalo halijawahi kutokea katika nchi hii. Narudi mwezi huu jimboni kwangu nikiwa nina uhakika wa bilioni 1; narudi nikiwa na uhakika wa shilingi milioni 600 kwa ajili ya ujenzi wa shule; na ninarudi ndani ya jimbo langu nikiwa na uhakika wa maboma 10 kwenda kuyatengeneza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, nina uhakika wa mradi wangu wa maji wa kutoka Mto Ruvuma kuja Mangaka utatekelezwa. Kwa kweli nampongeza sana sana sana Mheshimiwa Waziri kwa ubunifu mkubwa aliokuja nao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali, sasa tunarudi majimboni sisi Waheshimiwa Wabunge, mtuletee fedha hizi haraka. Huu Muswada tuupitishe ndugu zangu ili mwezi huu Julai na Agosti ambapo tutabaki majimboni, tuweze kusimamia fedha hizi zikafanye kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jana kulikuwa na issue ya transfer price; labda naomba nichukue nafasi hii kuwaeleze ndugu zangu transfer price ni nini na jinsi gani inatumika kwenye kuiibia Serikali. Transfer price ili iweze kufanyika lazima kuwe na Kampuni mama ambayo kwa lugha ya kigeni parent company na kuwe na subsidiary company. Sasa hii kampuni mama ipo nje ya nchi; hii kampuni nyingine subsidiary inakuja kwenye nchi yetu. Ndio inapokuja kufanyika transfer price na wenzetu Wahasibu walishaligundua hili, ipo standard kabisa International Financial Reporting Standard (FRX kama sikosei 12), inayozungumzia transfer price.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo ili wizi huu ufanyike hawa wanatumia njia mbili, ile kampuni mama ambayo iko kule labda nchi yoyote tuseme nchi “A”, inakuja kufungua mradi hapa labda wa uchimbaji wa madini, wizi wake unafanyika katika maeneo mawili. Moja, wana-over invoice, ku-over invoice services huku, ile kampuni mama imekuja kufungua machimbo ya madini kwetu, wale wanapotaka kutoa service katika ile kampuni yao ya huku, wanaichaji bili kubwa, wakiichaji bili kubwa wanapunguza kiwango cha kodi ambacho hii kampuni ambayo imefunguliwa hapa iweze kuilipa Serikali. Hiyo ni sehemu ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, sehemu ya pili kunakuwa na factitious payment, malipo hewa hewa, wanajifanya hii kampuni ya hapa inailipa ile kampuni mama kule, tumelipa hiki Board of Director, sijui tumelipa nini, anatumwa mtu kuja kutembelea hii kampuni analipwa ili kusafirisha fedha kule. Kwa hiyo ipo financial reporting standard, ambayo inasaidia kugundua mambo haya, wenzetu ma-auditors wakishaligundua hili.

Kwa hiyo inatakiwa kampuni hii inapofunga vitabu vyake i-disclose kama sisi ni subsidiaries company, kampuni mama ipo nchi Fulani. Asipofanya hivyo Auditor anakuwa na two option, moja anarudisha malipo yote yaliyofanyika kwenye ile kampuni mama kwamba sio halali, kwa hiyo yanatozwa kodi. Hata hivyo, kama amefanya inamlazimu sasa Auditor aangalie kwamba malipo haya yana uhaliali kiasigani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naishauri Serikali na naiunga mkono sana kama Mheshimiwa Mwigulu alivyosema, lazima tu-press signal, kwamba signal hii kwamba tunajua huu mchezo. Pili, wataalam wetu watambue kwamba sisi tunafahamu. Kwa hiyo mimi naomba ndugu zangu hii transfer price tuiachie Serikali na ile proposal yao, ili hawa wafadhili waweze kuja, pia tutakuwa na uwezo wa kuwabana. Watakaokuja kufungua makampuni hapa tutakuwa na uwezo wa kuwabana kama tunafahamu na hata wataalam wetu watambue kwamba tunajua kuna mchezo wa transfer price. Hilo la pili. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, Mheshimiwa Waziri alizungumzia masuala ya property tax na jinsi gani inatakavyokusanywa. Naunga mkono kwamba ile asilimia 15 yote ipelekwe TAMISEMI na ikishapelekwa TAMISEMI ndipo pale watakapoanza kuzigawanya kwenye halmashauri zetu. Mpango huu ni mzuri sana kwa sababu kuna baadhi ya miji ina property nyingi na kuna baadhi ya miji haina property za kuchaji hii property tax. Kwa hiyo, wazo la kukusanya na kupeleka TAMISEMI, halafu TAMISEMI wakatugawia kulingana na mazingira yetu, naliunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisisitize mifumo. Hivi karibuni tumegundua matatizo makubwa sana ya mifumo yetu, mifumo mingi imeingiliwa. Sasa kwa kuwa tunaingia katika utaratibu huu kuanzia mwezi ujao, naiomba Wizara iangalie mifumo hii iwe inasomeka. Leo TAMISEMI wana mifumo yao ya ukusanyaji wa mapato, Hazina wana mifumo yao ya ukusanyaji wa mapato na Bandarini wana mifumo yao ya ukusanyaji wa mapato. Sasa naiomba Wizara iisimamie mifumo hii iwe ni ya aina moja na isomeke, vinginevyo kutakuwa na athari ya kuleta hujuma katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja mia kwa mia ili mapato haya yatumike, yaweze kutuletea maendeleo katika Wilaya zetu. Ahsante sana. (Makofi)