Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Jafari Chege Wambura (27 total)

Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote kwanza nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi. Niseme tu kwa kuwa, hapo nyuma nilishapata nafasi ya kuchangia, hasa kwenye upande wa shughuli za kijamii, kwa maana ya maji, umeme na shughuli nyingine. Leo kwenye mpango nilitamani sana nijikite eneo moja la ardhi pamoja na makazi.

Mheshimiwa Spika, kwenye mpango natambua tumeiweka kwamba, Serikali ina mpango wa kuhakikisha angalao eneo lililosalia ambalo halijapimwa kwa ukubwa wa eneo letu zaidi ya 880,000 kilometa za mraba tumepima eneo zaidi ya asilimia 25 peke yake. Lakini kwenye mpango umetamka namna gani ambavyo kwa miaka hii mitano tunajikita kwa ajili ya kutambua, kupanga pamoja na kupima.

Mheshimiwa Spika, sasa nilitamani nishauri kwasababu, uliwahi kusema hapa ndani na mimi niendelee kuisema kama tukiitumia ardhi yetu vizuri, tukiipima vizuri ardhi yetu naamini kwa sababu, ni mdau wa sekta hii ya ardhi naamini inawezekana ndio kikawa chanzo kikubwa sana cha mapato ndani ya nchi yetu hii Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa nishauri? Nini tufanye kutokana na mpango uliopo? Cha kwanza. Ipo idara ambayo inasimamia shughuli za kupanga, kupima pamoja na kurasimisha ardhi ambayo iko chini ya Wizara ya Ardhi. Tulivyokuwa na changamoto ya maji vijijini tulianzisha chombo cha kushughulika na changamoto za maji, RUWASA. Tulivyokuwa na changamoto za barabara vijijini tulianzisha TARURA, tulivyokuwa na changamoto za umeme tulianzisha REA.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nashauri baddala ya kuwa na idara ambayo imejificha ndani ya wizara inayoshughulika na kupanga, kupima na kurasimisha haya maeneo, twende tuone namna gani tunatengeneza agency iwe wakala inayojitegemea ambayo kazi yake kubwa sasa iwe ni kupima na kuendana na mpango wa Serikali huu uliopangwa wa miaka mitano. Tukifanya hivyo, maana yake ni nini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza itakuwa na wigo mpana wa kushirikiana na sekta na taasisi nyingine. Hii migogoro tunayoizungumza ya ardhi kati ya wananchi na jeshi tukiwa na wakala anayejitanua maeneo yake maana yake atafanya kazi kubwa, lakini ataendana na kasi ya sisi tunayoizungumza kwamba, kwa muda mfupi asilimia 75 ya ardhi iliyosalia iweze kupimwa ndani ya miaka mitano.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili. Mpango ujikite uone namna gani unaweza ukashirikisha halmashauri moja kwa moja. Pamoja na kwamba, halmashauri nyingi zina vyanzo vingi vya mapato ningetemani sana mpango upeleke maelekezo moja kwa moja kwamba, halmashauri zirudi sasa zitambue kupanga na kupima maeneo yao ya ardhi, ili angalau moja kuongeza mapato, lakini mbili kama mnavyotambua tukipanga na tukipima eneo tunapunguza migogoro, kwa kufanya hivyo maana yake tutaipunguzia Wizara mzigo.

Mheshimiwa Spika, wizara sasa inafanya kazi kubwa sana ya kutatua migogoro badala ya kuibadioisha ardhi iwe source au chanzo cha mapato kwenye Serikali yetu. Ningetamani, sasa kwasababu Mheshimiwa Waziri ameshafanya kazi kubwa sana ya kukimbizana na migogoro aende aifanye sasa ardhi iwe ni sehemu ya kuongeza mapato, ili angalau mwisho wa siku tuweze wote kufaidika na sekta hii ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa miezi nane peke yake, kuanzia mwezi wa nane mpaka sasa Wizara imeingiza zaidi ya bilioni 93. Unaweza ukaona asilimia 25 ya ardhi iliyopimwa peke yake tuna bilioni 93, lakini asilimia 77 kati ya 880,000 ya ardhi ambayo haijapimwa tujiulize leo ardhi yote tukiipima kukawa na usimamizi thabiti ambao tukawa na mawakala ambao wanashughulika moja kwa moja na wanawajibika kabisa na upimaji na urasimishaji wa ardhi, Serikali itakusanya kiasi gani cha fedha kupitia sekta ya ardhi peke yake?

Mheshimiwa Spika, lakini la pili. Nizungumzie kuhusiana na hii ni Wizara ya Ardhi pamoja na Makazi, niende sasa kuzungumzia kuhusiana na nyumba. Wabunge wengi tumekuwa tukilalamika hizi real estate developers, National Housing, TBA na watu wengine ambao wamekuwa wakijenga nyumba kwa gharama kubwa. Na wengine tulikuwa tukihoji hapa kwamba, affordability ya nyumba inapatikana wapi?

Mheshimiwa Spika, haya yote tunashindwa kufika mwisho kwasababu, hatuna housing policy. Tunazo sera za misitu na sera za nyuki na sera nyingine, lakini hatuna sera inayotudhibiti na inayotuongoza kwenye nyumba, ili mwisho wa siku National Housing wakijenga nyumba Rorya, tukisema nyumba ni ya bei nafuu iwe angalau tayari ina limit kwa sababu, tukiwa na policy maana yake tutatengeneza sheria. Akijenga Rorya nyumba ya milioni 20 tutakuwa tunajua kabisa hii kweli milioni 20 ni affordable. Akijenga Kongwa nyumba ya milioni 20 tunaweza tukamhoji, hii ni affordable nyumba ya vyumba viwili?

Mheshimiwa Spika, kwasababu, kutakuwa kuna sheria inayomuongoza yeye katika ujenzi, sasahivi hakuna sheria. Anaweza akajenga nyumba akai-term kama affordable, ukimuuliza kwetu sisi, mimi inaweza isiwe affordable milioni 50, lakini kuna mtu mwingine milioni 50 kwake ni affordable. Na kwasababu hakuna policy wala sheria inayomuongoza inakuwa ni wakati mgumu sana kujua sasa wapi Serikali inasimamia kusema affordability ya nyumba ni ipi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na huu utakuwa ni muongozo mzuri kwa TBA, national Housing na real estate developers wengine wote wanaofanya shughuli za kujenga maeneo. Hata Serikali kwa maana ya kupitia Wizara itakuwa na sehemu ya kujivunia, unapokwenda ukasema unaonesha nyumba za affordability’s unaonesha kulingana na uhalisia uliopo.

Mheshimiwa Spika, sio uwongo gharama za ujenzi wa kila maeneo zinatofautiana. Gharama ya ujenzi wa Rorya haiwezi kuwa sawa na gharama ya ujenzi wa Dar-es-Salaam. Kwa hiyo, maana yake ile ukii-term kwamba, huyu mtu ambaye anajenga nyumba ajenge nyumba ya affordability Rorya ya milioni 30 ukasema sio affordable atakuuliza ni sheria ipi inayomuongoza? Kwa hiyo, ningependa nichukue nafasi hii kuiomba sana Wizara, lakini kupitia Waziri wa mpango, Waziri wa Fedha, ilia one namna gani ile sheria, ile policy inaweza kufanya kazi.

Mheshimiwa Spika, lakini la mwisho ni kwenye RERA, Real Estate Agency. Leo kuna watu sio vizuri kuwasemea, hawa tunaowaita madalali; brokers leo akiuza ardhi akiwa mtu wa kati hata kama ardhi ni ya milioni 500 akichukua commission hakuna kodi anayolipa. Lengo letu ni nini?

Mheshimiwa Spika, nilikuwa natamani sana tutengeneze Real Estate Agency, tutengeneze Real Estate Regulations ambazo zinawa-guide hawa ma-brokers na hawa ma-Real Estate Agency, ili mwisho wa siku moja itasaidia ku-regulate, lakini mbili itasaidia kukusanya kipato ambacho anashiriki kwenye kuuza kama mtu wa kati, lakini tatu itakuwa ni fursa kwao kufanya shughuli za kibiashara kwasababu, sasa watakuwa wanatambulika wako wapi. Leo ni ngumu sana kumtambua broker yupo wapi na anafanya kazi gani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana. Asante sana kwa kunipa nafasi. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Leo nitajitahidi kidogo nichangie taratibu ili angalau wote kwa ujumla hasa Wabunge ambao tumeingia ndani ya Bunge hili kwa awamu ya kwanza hasa Wabunge vijana, baada ya hapa ni imani yangu tutakwenda wote sambamba.

Mheshimiwa Spika, awali ya yote, nichukue nafasi kukushukuru sana wewe binafsi kwa namna unavyoliongoza hili Bunge. Nachelea kusema maneno haya kabla ukiwa ndani ya Bunge hili na ukiwa ni Spika wetu sisi kama Kiongozi wa Bunge. Ukistaafu ukiwa ndani ya Bunge hili ndiyo nipate ridhaa ya kukushukuru kwa namna unavyotuunganisha sisi Wabunge ndani na nje ya Bunge. Pia namna ambavyo unajitahidi angalau kumpa Mbunge mmoja mmoja nafasi ya kusemea yale ambayo anatakiwa ayasemee kwa mustakabali mzima wa wananchi ndani ya Jimbo lake. Mwenyezi Mungu pekee ndiyo anaweza kukulipa hili, muhimu ni kukuombea uzima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, nichukue nafasi kumshukuru sana Waziri Mkuu kwa namna anavyotuunganisha sisi Wabunge na Serikali kama Mtendaji Mkuu wa Serikali. Pia nichukue nafasi hii kuwashukuru Mawaziri wote kwa namna ambavyo pamoja na changamoto walizozipitia hapa katikati wiki tatu zilizopita, lakini bado wamebaki imara wanatuongoza na sasa tunakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nichukue nafasi kumshukuru Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan. Namshukuru kwa namna ambavyo ameanza, lakini namshukuru kwa namna ambavyo ameanza na anasema kazi iendelee kutekeleza na kulinda yale yaliyokuwa yanafanywa na pacha wake Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Ametuonesha sote kwamba njia bado iko pale pale. Yale waliyokuwa wanayasimamia juu ya wananchi maskini, miradi ya maendeleo, juu ya utendaji mkubwa wa Serikali kwa ujumla wake, bado ameahidi kuyasimamia na sasa tunaona kazi inakwenda vizuri. Ndugu zangu Wabunge tuendelee kumwombea mama yetu ili aendelee kufanya yale mazuri kwa kadri ambavyo Mungu ataweza kumwongoza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nirudi sasa kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Kwa mujibu wa Taarifa ya Shirika la Kifedha la Kimataifa la IMF mwezi Januari, kutokana na ugonjwa wa corona IMF ilikadiria uchumi wa kidunia utashuka kwa asilimia 3.5 kulinganisha na 2.8 ya mwaka 2019, lakini Serikali yetu juu ya Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli wakishirikiana na pacha wake, mimi namwita pacha mama yangu, mama Samia Suluhu Hassan kwa sababu hakuna namna unaweza ukazungumza mazuri yaliyokuwa yanafanywa na Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli bila kumgusa mama Samia Suluhu Hassan. Hakuna namna unaweza ukazungumza mazuri yaliyokuwa yanafanywa na hawa watu wawili bila kumtaja Waziri Mkuu kama Mtendaji Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo niseme, kwa namna ambavyo walituongoza pamoja na kushuka na kuyumba uchumi wa kidunia pato letu la Kitaifa la ndani ya nchi liliongezeka kwa asilimia 4.7. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kuwapongeza sana, Wabunge waliokuwa humu wanajua changamoto ilivyokuwa hasa baada ya tikiso hilo la ugonjwa wa corona, walibaki imara wakawasemea wananchi, sasa haya ndiyo matunda yake ambayo wanayaona. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niende sasa kwenye hotuba hiyo hiyo ya Waziri Mkuu. Taasisi ya Utafiti wa Kilimo kutokana na hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, imejipanga sasa kufanya utafiti wa kilimo wa kuangalia namna gani sasa tunaanza kubuni mbegu bora na miche bora kwa mustakabali wa wakulima wa nchi yetu. Nina mambo mawili au matatu ya kushauri.

Mheshimiwa Spika, watakapokuwa wanafanya utafiti huu, waende sasa wakatazame namna gani wanafanya utafiti kwa ngazi ya kimkoa, wilaya na halmashauri, washuke chini ngazi ya kata mpaka vijiji ndani ya nchi nzima, ili mwisho wa siku waje kulingana na jiografia ya kila eneo ni zao gani moja linafaa kulimwa kama zao la kibiashara.

Mheshimiwa Spika, pili, utafiti huo ujikite katika maeneo gani ambayo yanaweza yakalimwa na yakafanyika kilimo cha umwagiliaji na yakawanyanyua wananchi kwa ujumla kwenye kipato chao kwenye maeneo yote.

Mheshimiwa Spika, tatu, waende wakafanye utafiti warudi kushauri ili angalau sasa kwenye kila wilaya tuwe tuna zao moja la kibiashara ambalo wilaya moja ikisimama inasema ndani ya wilaya yangu, zao fulani ndiyo zao la kibiashara ambalo kimsingi kama Mbunge nikitaka kuwashika mkono kuwasaidia wale wananchi mbegu nawasaidia mbegu ambayo wanajua wakiipanda kama zao la kibiashara itainua uchumi wa wananchi kwenye maeneo yao husika.

Ningetamani sana, tafiti hizi ninaporudi ndani ya Jimbo langu kwenye wilaya nione kwamba kweli hapa kwenye kata fulani ndani ya kijiji Fulani, nikiwashauri wananchi kulima pamba inastahimiliki na isiwe kwa ku-guess au kwa kuchukua yale maoni ya wakulima peke yake, badala yake, niweze kuitoa hata kwenye taarifa za utafiti huu utakaokuwa umefanywa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, hapo hapo kwenye kilimo ningetamani sana, kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru sana Waziri wa Kilimo kwa namna ambavyo amejipanga kupeleka pikipiki kwa Maafisa Kilimo wote ndani ya halmashauri. Wasiishie hapo tu, ningetamani waende moja kwa moja, watengeneze mustakabali mzuri wa kuwasimamia Maafisa Kilimo ili Afisa Kilimo anapoamka asubuhi, ajue ni mashamba mangapi anakagua kwa siku, ametembelea wakulima wangapi, anategemea kupata nini kwa wale wakulima. Mwisho wa siku wampime kwa product inayopatikana kwenye ngazi ya chini kabisa, ngazi ya Kijiji, itakayoleta tija, lakini itaamsha ari mpya ya utendaji wa Maafisa Kilimo kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, natamani sana Wizara ya Kilimo pamoja na kwamba tunawapelekea vitendea kazi, tufike tutengeneze assessment nzuri ya kuwasimamia ili ninaposimama hapa kama Mbunge, yakitajwa maeneo mengine, nami nikitaja kama Rorya nataja mazao fulani ambayo wananchi wangu wameyapata kwa mwaka mmoja kwa kilimo walichokifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo nizungumzie kuhusu huduma za kijamii na nitaanza na maji. Nichukue nafasi hii kwanza kumshukuru sana Waziri wa Maji. Nasema ni katika Wabunge wachache ambao baada ya yeye kupata uteuzi alifanya ziara kwenye jimbo langu. Kulikuwa na Mradi wa pale Shirati, mradi ulikuwa na zaidi ya miaka 10 hautoi maji, lakini alipofika alitoa maneno ndani ya mwezi mmoja, ninavyozungumza chini ya Serikali hii ya Chama Cha Mapinduzi, leo kuna maji yanatoka pale. Unaweza ukaona ni historia gani ndani ya miaka 10, wananchi wale walikuwa wamesahau issue ya maji, leo wanapata maji.

Mheshimiwa Spika, sasa nikuombe Mheshimiwa Waziri pale imepelea kiasi cha kama milioni 300, najua hili unaliweza, tusaidie ili tuweze sasa isiwe Shirati peke yake badala yake na majirani wote wanaozunguka kata ile waweze kupata maji kwasababu, miundombinu ipo ni kuifufua tu iweze kuwasaidia wananchi kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Spika, lakini pia kuna miradi ya maji ambayo iko ndani ya jimbo. Nichukue nafasi hii kukuomba kuna miradi ya Nyarombo, kuna miradi kwa muge pale Kyang’wame na miradi mingine ambayo kimsingi ukiwekeza fedha pale itawsaidia sana wananchi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri tusiishie mradi mmoja, turudi tuone namna gani ya kuwasaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niliwahi kusema na nitarudia tena, ili kutatua changamoto ya maji ndani ya Jimbo ni lazima twende na ule mradi mkubwa wa maji ambao upo kwenye plan ya kutoa maji Rorya kwenda Tarime. Ule mradi tunazungumzia zaidi ya kata 28 zitanufaika na ule mradi na kwa sababu, jimbo langu zaidi ya asilimia 50 changamoto kubwa ni maji ni imani yangu huu mradi ukiingia kwenye pipeline ukaanza kutekelezwa Rorya issue ya maji itakuwa ni historia. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kwa unyenyekevu mkubwa sana na kwa sababu limesemwa na Waziri Mkuu ni imani yangu litafanyika vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu nikuombe, ni imani yangu kipindi mlikuwa mnatunadi sisi Wabunge vijana, Wabunge ambao tumeingia kwa mara ya kwanza, mlikuwa mnazunguka wewe, Spika, Mheshimiwa Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli na Mama yangu Mama Samia Suluhu Hassan. Ulipopita kwenye jimbo langu uliniahidi namna gani tunaweza tukapata ambulance, ili angalau iweze kusaidia wale wananchi. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwenye hili tusaidie.

Mheshimiwa Spika, la kumalizia la mwisho nimalizie kuhusiana na issue ya TARURA, tuna daraja pale la Mto Mori, kwa sasa hivi kwasababu nimemuona Waziri wa TAMISEMI amekuja mama na lile daraja tunazungumzia kipenyo ambacho hakizidi hapa na Mheshimiwa Waziri alipo upana wa lile daraja. Ni imani yangu kwasababu limekuwa likizungumzwa zaidi ya miaka 10 huku nyuma sasa amekuja Waziri ambaye ni mama na ninaamini ni mchapakazi mzuri sana wanaoteseka kuvuka kwenda kutafuta huduma za kijamii, huduma za hospitali, huduma za masoko ni akinamama na watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na niliwahi kusema mto ule watu wamekuwa wakifariki pale. Angalia kipenyo tunachohitaji daraja ambalo tumekuwa tukiliomba kwa miaka 10 ni hapa na pale alipo Mheshimiwa Waziri. Ni imani yangu sasa amekuja mama atawasaidia hawa wamama ili lile daraja sasa badala ya kila mwaka kufanyika upembuzi yakinifu liweze kupata suluhisho la kudumu ili hawa wananchi sasa waweze kuokoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia la mwisho kabisa nizungumzie kwenye sekta ya afya kwenye upande wa Waziri.Ndani ya jimbo langu nina kata 26 ni kata tatu tu ambazo zina vituo vya afya na bahati mbaya sana Kata ya Kinesi ambayo ina Kituo cha Afya cha Kinesi kwa mujibu wa projection ya Wizara ilitakiwa ihudumie vijiji viwili peke yake. Hivi ninavyozungumza kituo kile cha afya kinahudumia zaidi ya vijiji 27 zaidi ya tarafa tatu wanapata huduma tena mpaka Kijiji Jirani cha Butiama, watu wanaokwenda pale projection yake imekuwa ni kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, na kwasababu kimeshapanuka na Serikali ilitupa fedha tukakipanua zaidi ya milioni 500 hapa kilipofikia nichukue nafasi hii kumuomba sana Waziri tuone namna gani sasa tunakihamisha kwasababu, kimeshatoka kwenye vigezo vya kutoa huduma kama kituo cha afya kiende kiwe hospitali ya wilaya ili angalao tuweze kuwa na hospitali ya wilaya kwa ukanda wa chini upande wa Suba. Na hii hospitali ya wilaya ambayo Serikali ipo kwenye mchakato wa kuifungua upande wa pili maana yake tutakuwa na hospitali mbili, angalau kwa jiografia ya jimbo langu lilivyokaa tunaweza tukawasaidia sana wale wananchi kwenye sekta ya afya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya haya machache nichukue nafasi hii na niseme kwamba, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwanza kwa kunipa nafasi. Nianze tu kusema kwa kuchangia Wizara ambayo binafsi nimeitumikia kwa zaidi ya miaka kumi. Naweza nikasema tu kwa wepesi kwamba nimepata nafasi ya kuchangia Wizara ambayo imenilea kabla ya kuwa mwanasiasa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nitumie nafasi hii kuwashukuru; wa kwanza kabisa Mheshimiwa Waziri, ndugu yangu, mzee wangu, Mheshimiwa William Lukuvi; Naibu Waziri, mama yangu, Mheshimiwa Dkt. Angeline Mabula. Pia nitumie nafasi hii kumshukuru Katibu Mkuu wa Wizara hii, dada yangu Mary Makondo na Naibu wake.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitawashukuru wafanyakazi na watendaji wote wa Wizara hii walioko ndani ya Wizara na wale ambao wanafanya shughuli kama wadau, kwa maana ya private sector. Haya mafanikio ambayo tunayaona ya Wizara hii, mimi kwa sababu nimekuwa kule natambua mchango mkubwa wa watu wote kwa ushiriki wao kwa pamoja ili kuhakikisha angalau tunaisukuma Wizara yetu hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitakuwa na maeneo matatu, nafasi ikiniruhusu nitakuwa na eneo la nne la kuchangia kwenye Wizara hii. La kwanza niombe nichangie kwenye ushiriki wa private sector kwenye Wizara hii ya Ardhi. Nianze kwa kusema kwamba ili mwananchi aweze kumilikishwa ardhi, maana yake kuna vitu vitatu au vinne vinakuwa vimefanyika; cha kwanza ni lazima ardhi iwe imepangwa; maana yake katika kupangwa ndiyo kutaainisha matumizi bora ya ardhi ile.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili, ardhi lazima iwe imepimwa. Kwenye kupimwa ndiyo tunapata ukubwa wa ardhi na maboresho mengine ili mwishoni mwananchi aweze kumilikishwa ardhi ile. Kwa haya matatu tokea Uhuru, toka mwaka 1961, ardhi ambayo imepangwa mpaka sasa tunavyozungumza ni zaidi ya viwanja milioni sita peke yake. Kati hivyo milioni sita, viwanja ambavyo vimepimwa kwa maana ya kwamba sasa vinakwenda ili viweze kupewa ardhi, ni milioni 2.5. Viwanja ambavyo mpaka sasa tunazungumza kwa maana ya umiliki wa mwananchi mmoja mmoja ni milioni 1.5.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushiriki wa private sector kwa mwaka 2015 kwenda 2020 ndiyo tumeanza kufanya shughuli ya urasimishaji kwenye maeneo yetu. Hawa watu, hizi private sector unaweza ukaona katika hiyo milioni sita ambayo ni miaka zaidi ya sitini katika kupanga matumizi ya ardhi, wao wameweza katika urasimishaji peke yake, katika milioni sita maana yake kuna viwanja milioni 1.6, hizi private companies, makampuni ya watu binafsi wameweza kuisaidia Serikali, kwa miaka mitano.Kwa miaka mitano wameweza kupima, kupanga ardhi viwanja zaidi ya milioni 1.6. Lakini total zaidi ya miaka sitini ni zaidi ya viwanja milioni 60; hilo ni la kwanza tu peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, katika kupima peke yake kwa miaka mitano toka 2015 hadi 2020, zaidi ya viwanja 557,000 ambavyo vimepimwa katika kazi ya urasimishaji na hizi private companies.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwa kutambua mchango huu pamoja na kwamba amezungumza yapo makampuni ambayo hayafanyi kazi vizuri, tukae nao tuone yale makampuni katika makampuni 163, yale manne ambayo mwanzoni amekuwa akiyasema hayafanyi kazi vizuri, yale 159 twende nayo. Tukiwaweka pembeni hawa tutambue kwamba hawa ndio wana kazi kubwa sana ya kutusaidia sisi. Unaweza kuona kwa miaka mitano namna gani wmaeingia katika shughuli ya kupanga, kupima na mwishoni wakaenda kwenye kurasimisha, namna ambavyo wamefanya kazi kubwa sana. Tusiwahukumu wote kwa pamoja, twende kwenye yale makampuni mengi ambayo yamefanya kazi vizuri tuweze kwenda nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nilikuwa namsikiliza Mheshimiwa Waziri wa Kenya, siyo vizuri kusema lakini naomba nitoe kama mfano, alikuwa anazungumza kwa miaka mitano (2015-2020) wao kwa kutumia private sector wameweza kupima viwanja zaidi ya milioni tano. Unaweza ukaona wao wamejikita sana kutumia private sector kwa miaka mitano wamepima viwanja milioni tano. Sisi toka Uhuru bado tuna milioni sita peke yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiziacha hizi private companies zote tukazihukumu katika mfumo huo maana yake ni kwamba Serikali peke yake ndiyo itaingia kufanya hiyo kazi. Sisi wote tunatambua Waheshimiwa Wabunge, watumishi kwenye halmashauri hawatoshi. Kwa mfano Rorya nina mtumishi mmoja tu Afisa Ardhi. Maana yake sina Mpimaji wala sina mtu wa Mipango. Maana yake tukiwaachia wao wafanye kazi hizi hatutaweza kufikisha malengo, lakini pia hatutatimiza Ilani ya Chama Cha Mapinduzi katika ukurasa wa 119 ambao umesema kwa muda mchache ili twende na kasi ya kupima maeneo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia tutambue kwamba kampuni hizi zimetoa ajira kwa vijana wetu. Kampuni hizi ambazo leo hii tukiziacha pembeni zimekopa mikopo, tukiziacha pembeni zisifanye shughuli hii tutakuwa hatuwatendei haki na yawezekana tukaanzisha mgogoro mkubwa sana kwenye sekta ya ardhi huko mbeleni tunakoelekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni ushiriki wa halmashauri. Kwa mujibu wa sheria mwenye mamlaka ya upangaji nchi hii ni halmashauri. Hata hivyo, twende mbele turudi nyuma, kazi hii tumeona imebaki ikifanywa sana na Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi wakati tunapitisha bajeti ya Wizara ya TAMISEMI tuliona ndani mle, nilikuwa naona moja ya vipaumbele vyake ni kuhakikisha ardhi yote inapimwa. Hata hivyo, ulikuwa ukienda kwenye bajeti kuona kwamba namna gani wanakwenda kufanya kazi hiyo kama Wizara ya TAMISEMI, hakuna fedha iliyotengwa kwa ajili ya kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo tukirudisha kwamba halmashauri peke yake kwa sababu kwa mujibu wa sheria ndiyo wana mamlaka ya kupanga na kupima wafanye kazi kwa kupitia mapato yao ya ndani, mathalani mimi Rorya nakusanya milioni 800 tu kwa mwaka. Milioni 800 nichukue asilimia 40 iende kwenye shughuli za maendeleo, bado niitoe iende kwa ajili ya kupima ardhi. Hawatakwenda na kasi tunayoizungumza ya miaka mitano ya utekelezaji wa Mpango na Ilani ya Chama chetu Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha aone namna gani anaiongezea fedha Wizara ya Ardhi, hasa kwenye kipengele hiki cha upimaji ili hizi halmashauri huko chini ziingie kwenye uratibu na kutafuta namna ambayo wanaweza wakapima ardhi kuendana na kasi ya Wizara namna inavyotaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kuomba sana kwa sababu kama kweli dhamira yetu ni ya pamoja, kwamba angalau sasa zaidi ya eneo la kilometa za mraba 883,000 tumepima asilimia 25 peke yake, tukiiachia Wizara peke yake iendelee na huo mfumo na kwa kutoa maelekezo kwa halmashauri zitafute fedha zenyewe ziende kupima, hatutakuwa tumewatendea haki hawa wananchi wetu. Lakini pia hata Serikali bado tutakuwa tunaimba wimbo uleule na inawezekana tusifikishe malengo yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ni ushiriki wa Tume ya Taifa ya Mipango na Matumizi ya Ardhi. Moja ya majukumu ya Tume hii ni kuwezesha mamlaka zote za upangaji wa matumizi ya ardhi katika kutambua mipango ya matumizi ya ardhi, zikiwemo halmashauri zote. Ukienda kwenye bajeti unaweza ukaona tume hii, ndiyo maana miaka yote watu wengine wamekuwa wakisema hatuoni tija ya tume hii, lakini inafanyaje kazi? Unaweza ukaona kwenye fedha ya maendeleo imetengewa bilioni 1.5 peke yake, namna gani itaweza kufanya kazi hii?

Mheshimiwa Naibu Spika, ndiyo maana nilikwenda mbele nikashauri kwamba kama kweli tuna mpango tumejikita kama Serikali na nchi kwa ujumla tunataka tuhakikishe tunapima ardhi kwa muda mfupi, ni lazima tutengeneze agency. Agencies kama ilivyo TBA, lazima tuwe na wakala ambaye anahusika na shughuli zote za kupanga na kupima ardhi. Ili tunapokwenda kumpangia fedha kwa muda mfupi awe na fedha nyingi lakini utekelezaji wake utakwenda kwa kasi kama ilivyo TBA ambayo ni utekelezaji wa nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo agencies, wapo mawakala wengi ambao wanafanya kazi kwenye maeneo mengine. Ili tuondokane na hili na ili tuendane na mpango wa miaka mitano kwa kasi, ni lazima tutafute namna ambayo tutaiongezea fedha Tume ya Taifa ya Mipango, lakini tutengeneze agency, shughuli ya kupanga na kupima ardhi isibaki kwenye kurugenzi moja tu peke yake ndani ya Wizara, tujaribu namna ya kuipanua ili iendane na kasi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, naomba nizungumzie kuhusiana na makazi. Wabunge wengi tumekuwa tukitoa mawazo na michango mingi sana inajikita kwenye ardhi, lakini hatuendi sana kutafuta namna ambavyo tunaweza tukapata suluhu ya upande wa nyumba ili hiyo concept ya Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi iweze kujaa vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitumie nafasi hii kushauri na pia niweze kuunga mkono maoni ya Kamati kwamba angalau kwa mwaka huu kama ikipendeza, Wizara iweze kukamilisha Housing Policy, Sera ambayo itaratibu shughuli za ujenzi wa nyumba. Hapa Wabunge wengi tumekuwa tukisema namna ambavyo mashirika, kwa mfano, Shirika la Nyumba na Taasisi nyingine, zinajenga nyumba kwa bei kubwa sana. Hata hivyo, leo tukiulizana humu ndani bei elekezi ya ujenzi wa nyumba, mfano Rorya, hatuitambui. Kama tukiwa na Housing Policy maana yake ni nini? Itakuwa na maelekezo ya ujenzi wa nyumba kuanzia ngazi ya mkoa, wilaya na maeneo yote ili hawa wanaojenga nyumba watakuwa wanajenga kwa kutambua bei elekezi iliyopangwa kwenye maeneo yote.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwa mwaka huu angalau sasa tuwe na policy ambayo itatuongoza sote kama Taifa ili tukizungumza Sera ya Nyumba tuwe na Sera ya Nyumba kama zilivyo sera za nyuki na nyingine. Hili litakuwa ni jambo zuri ambalo kimsingi naamini yale maoni mengi ambayo tumekuwa tukiyasema hapa Bungeni namna ya ku-regulate bei za ujenzi wa nyumba itakuwa vizuri na tutakuwa tumei-control vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri, tumekuwa tukiongea naye mara kwa mara; kuna wananchi wangu kule walifanyiwa uthamini toka 2011 Rorya, nafikiri hili analifahamu. Niombe atakapokuwa anakuja kufanya majumuisho angalau na wao wapate jibu. Toka 2011 wamefanyiwa uthamini ili kupisha huduma za umeme, lakini mpaka leo ninavyozungumza kama ambavyo huwa nakwambia wale wananchi hawajalipwa fidia. Ni zaidi sasa ya miaka kumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri, anajua kwa mujibu wa sheria baada ya miezi sita, valuation ile ilitakiwa ipitwe na wakati. Nitumie nafasi hii kumwomba sana Mheshimiwa Waziri atakapofanya majumuisho alizungumzie hili ili na wao waweze kusikia.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Nianze tu kwa kusema ukisikiliza toka asubuhi mijadala ya Bunge letu hili Tukufu, Bunge la Kumi na Mbili, lakini pia ukisikiliza wadau wanavyozungumzia hasa kwenye wizara na sekta nzima ya elimu; utagundua wote tunajikita kwenye sera ya elimu yetu ilivyo kwa maana sera ya mwaka 2014.

Mheshimiwa Spika, pia tunazungumzia mfumo wa utoaji wa elimu nchini namna ulivyokaa. Ukisikiliza hotuba ya Mheshimiwa Rais, alivyozungumza juzi kipindi anahutubia Bunge, amezungumzia namna Serikali ilivyojikita kwenda kupitia Sera ya Elimu Nchini. Hata hivyo, sote hapa ni mashahidi huko tunapotoka kwenye majimbo, kwenye maeneo yote ya mijini, namna ambavyo wananchi na wadau mbalimbali wamekuwa wakizungumzia muundo na Sera ya Elimu ilivyokaa na namna gani ambavyo wameshauri jinsi ya kutoka hapa.

Mheshimiwa Spika, kabla sijaenda kwenye kuchangia. Naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kwenye majumuisho yake, kwa sababu leo tunajikita kwenye bajeti, basi kama haitatupendeza, Bunge hili la Kumi na Mbili kwa mikutano inayofuata Mheshimiwa Waziri waende kama Serikali, waende wakaanze mchakato wa kukaa na wadau, kuona namna gani ya kuifumua Sera ya Elimu na mfumo mzima wa elimu namna ulivyokaa ili Bunge linalofuata kwa maana kikao kinachofuata iwe kama section, iwe ni sehemu maalum ya kujadili namna ya mfumo na Sera ya Elimu jinsi ilivyokaa, kwa sababu pale tutakuwa na uwanja mpana wa kujadili elimu yenyewe kama ilivyokaa Nchini Tanzania.

Mheshimiwa Spika, pili, tutakuwa tunazungumzia yale ambayo wao wamekaa na wadau angalau wamepata mawazo yote kwa ujumla ili Bunge lako Tukufu, hili Bunge la Kumi na Mbili, tutoke na maazimio namna gani tunakwenda kufumua mfumo mzima wa elimu ili tutakapokuwa tunazungumza kama Wabunge tuwe angalau tumeshiriki kwenye hili ambalo kimsingi ukitazama kila mtu anayezungumza, anazungumzia namna ya mfumo na sera jinsi ilivyokaa ya utoaji elimu nchini.

Mheshimiwa Spika, naomba sana Waziri atakapokuja angalau atuahidi hiyo, kwamba angalau baada ya Bunge hili watakapokwenda waweze kuangalia namna gani tunaweza tukarudi mara ya pili kwenye vikao vinavyofuata ili tuweze kulijadili hili kwa upana wake na kwa ujumla ili tutoke na kitu kimoja kama Taifa ambacho kitakuwa na mustakabali mzuri wa kutuongoza kwenye sekta ya elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya maoni hayo, nirudi tu kuzungumzia masuala baadhi ndani ya jimbo langu. Nilikuwa natamani sana Wizara ya Elimu na Wizara ya TAMISEMI wafanye kazi kwa ukaribu sana kwa kushirikiana. Leo ulikuwa unazungumza hapa asubuhi, kuna mahali ukienda ndani ya jimbo langu mathalan, mimi nina shule mbili ambazo moja imejengwa tangu 2005, wamejenga wananchi kuanzia msingi. Wamejichangisha wenyewe wamejenga msingi, wamejenga maboma zaidi ya matano kule, lakini namna ya kupewa idhini sasa ya kufunguliwa iwe shule, kwa maana ya kufanya usajili mpaka leo ninavyoungumza hawajapewa usajili. Kila wakienda kwa hawa mabwana ambao wanajiita watu wa ukaguzi wanawaambia bado ongezeni majengo mawili. Unaweza ukatazama maboma matano na choo na ofisi za Walimu wamejenga wananchi, hapa Wabunge wengi wanatoka maeneo ya vijijini wanajua namna inavyokuwa kwa wananchi wakati mwingine kwenye kuchangishana ili kujenga haya maboma.

Mheshimiwa Spika, wakati mwingine mtu ana-sacrifice, alikuwa ana shilingi elfu moja, anaacha kwenda kununua mboga yake, kununua mahitaji yake ya ndani anachanga ili aweze kujenga ile shule. Badala yake wanapomaliza bado hatuwezi kuwapa usajili kwenye shule hii. Nini maana yake? Unakuta shule nyingine ambayo mwanafunzi anatakiwa kwenda ipo zaidi ya kilomita tano kutoka maeneo wananchi wanapoishi na wakati mwingine katikati ya maeneo hayo kati ya shule na wananchi wanapoishi kuna majaruba ya maji. Ili mwanafunzi huyu wa miaka saba au nane aweze kufika kule wakati mwingine wakati wa mvua inamlazimu kupita kwenye yale majaruba. Wananchi kwa kutambua umuhimu huo wakaamua kujenga shule yao. Leo ukiwaambia huwezi kuwasajilia na wakati ni suala la kuzungumza kati ya Wizara ya Elimu na TAMISEMI tukaona namna gani tunawasaidia, tunakuwa hatuwatendei haki wananchi hawa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri, atakapokuwa ku-wind up anisaidie kwenye shule zangu hizi mbili hizi; kuna Shule ya Tacho ipo Kata ya Kirogo na Shule ya Kuruya ipo Kata ya Komuge. Hizi ni shule ambazo zimejengwa na wananchi; hivi ninavyozungumza maana yake Shule ya Kuruya hata wanafunzi hawajakwenda mwaka huu, wameambiwa hatuwezi kuwapa wanafunzi kwa sababu haijasajiliwa, lakini wamejenga wananchi kwa kuepuka huo umbali wa kusafiri muda mrefu. Niombe sana Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anafanya majumuisho angalau wananchi nao wapate ahueni kutokana na nguvu zao ili mwisho wa siku wasije kuona nguvu zao zimetumika bila ya kuwa na maana yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili, naomba sana, Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anafanya majumuisho angalau apitie yale madai mbalimbali ya Walimu. Walimu wamekuwa na manung’uniko mengi sana na naamini kabisa hili lipo ndani ya uwezo wa Waziri. Manung’uniko haya anaweza akayatatua kwa muda mfupi sana. Wananchi wengi, Walimu wengi wamekuwa wakilalamikia miundombinu yao; maeneo wanayofundishia siyo rafiki kwao, lakini wengi wamekuwa wakilalamikia madeni ya likizo na madeni mbalimbali ya malimbikizo ambayo yamelimbikizwa huku nyuma. Naamini kupitia Mheshimiwa Waziri kwa sababu tayari nimeambiwa alikuwa ni Mwalimu na alikuwa Mwalimu mzuri ataweza kuwasaidia katika hili.

Mheshimiwa Spika, pia wana madai ya likizo ambazo walikuwa nazo. Ni imani yangu Mheshimiwa Waziri atawasaidia hili. Pili, tunapofanya mabadiliko ya mtaala, tunapowapelekea Walimu niombe sana tutengeneze fedha angalau za kuwatengezea capacity building, tuwajenge ili waendane na ule mtaala mpya tunaowapelekea. Kwa sababu unapobadilisha mtaala Mwalimu bado alikuwa anajua skills za nyuma zilizopita, ukimbadilishia anapata wakati mgumu sana kuendeana na ule mtaala mpya ambao umeupeleka kipindi hicho. Tuweze kuwapa mafunzo ili waendane na mtaala mpya ambao tumewapelekea. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho kabisa, ningependa sana kuzungumzia kuhusiana na ujenzi wa Vyuo vya VETA. Mimi Rorya nimepaka na Tarime, population ya haya majimbo mawili au hizi halmashauri ni zaidi ya watu 600,000. Hata kama bado Serikali inajipanga namna gani ya kupeleka Chuo cha VETA kila halmashauri, tuwekeeni chuo kimoja hata ukiweka pale VETA katikati ya Tarime na Rorya angalau tuweze kuwasaidia wanafunzi wote wanaotoka ndani ya halmashauri zote mbili…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Chege.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nikushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niungane na wenzangu kwanza kabla sijaenda mbele zaidi, kumshukuru na kupongeza kazi kubwa aliyoifanya na Rais wetu wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamesimama hasa wazoefu, wengi wamekuwa wakisema hii ni bajeti ya kumi; wengine ni bajeti ya tano kwa kadri ya muda wa miaka aliyokaa ndani ya Bunge. Sisi Wabunge ambao ni awamu yetu ya kwanza tunasema hii ni bajeti yetu ya kwanza. Kipekee kabisa tunakwenda tarehe 29 kwenye Majimbo yetu tukiwa tumetosheka na tumeshiba sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo ambayo kimsingi pamoja na miaka yote hii ya nyuma hayakuwa yakifanyika, sisi ndani ya Bunge hili kwa mara ya kwanza tunakwenda kwa wananchi wetu tukiamini na tukiyaona yamefanyika, angalau tunaweza tukasema nini Mheshimiwa Rais wetu ametutendea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumshukuru sana na pia kuwapongeza Mawaziri wote; Waziri Mwigulu Nchemba na Naibu wake pamoja na Wizara nzima, kwa namna ya kipekee walivyokaa humu ndani na kusikiliza maoni ya Wabunge. Leo hii ukiangalia upande wa TARURA, ni historia, haijawahi kutokea kutengwa fedha zaidi ya shilingi milioni 500 kurudi kwenye Majimbo, halafu Mbunge ukashirikishwa namna ya utendaji wa fedha ile. Haijawahi kutokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi tangu nimeingia hapa na nimekuwa nikilia sana juu ya daraja langu la mto Mori, na nimekuwa nikisema lile daraja linaunganisha tarafa tatu kati ya tarafa nne ndani ya Jimbo, hata tarafa ya nne nayo inaingia. Leo hii ninavyochangia hapa, nakwenda tarehe 29 ndani ya Jimbo nimepewa zaidi ya shilingi milioni 950, kwa ajili ya utekelezaji wa daraja lile. Nikiongeza na shilingi milioni 500 maana yake nina 1.4 billion, ambayo inakwenda kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo ndani ya Jimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nasema inawezekana ikawa ni bajeti ya kwanza kwa awamu hii, lakini kwetu sisi Wabunge wa mara ya kwanza kiukweli imetutendea haki na imetunyanyua sana. Pia amekwenda maeneo mengi; maeneo ya maji imegusa, maeneo ya afya imegusa, kiukweli sina namna ya kusema zaidi ya kuwapongeza Mawaziri na Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha muhimu ambacho nataka nichangie leo ni kumwomba Mheshimiwa Waziri, mimi napenda sana kushauri kuliko kusifia, kwa sababu naamini nikishauri vizuri ndiyo ataendelea kufanya kazi sawa sawa na ataendelea kuwepo kwenye Wizara hii na mwishoni atatengeneza historia ndani ya nchi hii ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Naomba niende ndani ya vipengele vya kumshauri ili aendelee kufanya kazi vizuri kuliko kumsifia zaidi. Naamini ameshafanya mengi mazuri, Wabunge wameshamsifia na anastahili sifa hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza ili kuhakikisha fedha zote za miradi ya maendeleo, tengeneza historia kuhakikisha fedha zote zilizotengwa zinakwenda kwenye majimbo na kwenye Halmashauri. Ukifanya hivi utakuwa umetengeneza historia ya miaka yote ambayo tunasema zinakwenda asilimia 10 na asilimia kadhaa kwenye bajeti za kisekta. Peleka fedha zote kwenye miradi ya kimaendeleo. Amini ninachokwambia Mheshimiwa Waziri, tukirudi hapa mwakani utakuwa umetengeneza historia nzuri sana, kwa sababu miradi mingi itakwenda kutekelezwa na mwishoni wewe ndiye utakayepata sifa hizi kwa wananchi wetu ndani ya maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, napenda sana kuchangia kwenye Property Tax (Kodi ya Majengo). Nishawahi kusema nachangia kama mdau. Ningependa nichangie maeneo matatu na ninaamini kwamba Mheshimiwa Waziri utalichukua hili, utakuja kulitolea ufafanuzi. Unakuta kwenye kiwanja kimoja, mimi mmiliki wa nyumba nimejenga nyumba tatu kwenye kile kiwanja au nyumba nne ndani ya kiwanja; nimeweka Luku moja peke yake. Maana yake mwishoni nikilipa Luku, nalipia nyumba moja. Sheria inavyosema, ni kila property; nyumba iliyopo kwenye kiwanja kimoja, kama ni property Na. 5 zile nyumba tatu zote kwa sasa zinalipia kodi ya jengo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ikiwa Luku ni moja kwenye eneo lile, lazima angalau utakapokuja Mheshimiwa Waziri utuambie, zile nyumba mbili zinazosalia katika tatu kwenye kiwanja kimoja, ni mpango gani mkakati uliopagwa ili angalau zote ziwe accommodated kwenye Luku moja ya ukusanyaji wa eneo hilo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwenye Property Tax kuna haya majengo, tuchukulie nyumba za ibada ambazo kimsingi kwenye sheria ya sasa hazikuwa zinalipa kodi. Kuna wazee wa miaka 65 na kuendelea, umri wao umezidi walikuwa hawalipo hii Property Tax. Namna gani sasa unaenda kuwa-accommodate? Kwa mfano, majengo haya ya ibada yana Luku: Je, hawatahusika kwenye Luku zao kulipia Property Tax? Nafikiri hii na yenyewe kwenye mkanganyiko Mheshimiwa Waziri utaiweka sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kuna majengo ambayo yanalipiwa na wapangaji. Mwenye nyumba amejenga, Luku inalipiwa na mpangaji: Je ni namna gani ambavyo tutawa- accommodate wale wapangaji ambao wananunua Luku kwenye majengo waliyopanga, wakati Property Tax inatakakiwa kulipiwa na mmiliki wa eneo lile (owners)? Haya mambo matatu Mheshimiwa Waziri naamini ukiyaweka sawa sawa hakuna kinachoshindikana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, nichangie sana kulingana na Mahusiano ya Hali ya Uchumi na Mpango wa Maendeleo ya Taifa, Mheshimiwa Waziri tutakubaliana, ili maeneo yote kuwe kuna uchumi imara kwa wananchi, cha kwanza kabisa, lazima kuwe na stability, lazima kuwe na usalama wa wale wananchi ili kufanya biashara vizuri. Nitatolea mfano ndani ya eneo langu mimi la Rorya. Mimi shughuli zangu za kiuchumi ni tatu; moja, ni kilimo; pili ni uvuvi na tatu ni ufugaji. Kilimo sina shida kwa sababu naamini kwenye bajeti ya kisekta Waziri amenitengea fedha na nitakwenda kutekeleza hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zinabaki shughuli mbili za kiuchumi ili wananchi wale ndani ya Jimbo waweze kwendana na kasi ya mpango wa Taifa ndani wa miaka mitano. Tuchukulie mfano suala la uvuvi. Mheshimiwa Waziri mimi kule, napenda nilizungumze kwa Waziri wa Bajeti, Waziri wa Fedha na pia Waziri wa Mambo ya Ndani na ikibidi Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kuna wizi mkubwa sana unafanyika kwenye maeneo ya maziwani. Wavuvi wanapokwenda kuvua na ndiyo shughuli kubwa ya kiuchumi. Ndani ya Jimbo langu Mheshimiwa Waziri, asilimia 77 nimezungukwa na ziwa. Unaweza kuona, ili uchumi wa wananchi wangu uweze kuendelea, ni lazima wafanye shughuli ya uvuvi, lakini haufanyiki sawa sawa. Wanapokwenda kuvua, wanakutana na shughuli kubwa sana ya kupigwa na kunyang’anywa zana zao za uvuvi. Nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani, ikibidi Waziri Mkuu atusaidie sana kwenye hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndani ya shughuli mbili hizo nilizosema, ya tatu ni ya ufugaji. Mheshimiwa Waziri, leo ufugaji haupo stable. Kule ndani ya Jimbo langu, kila siku ndani ya Halmashauri ya Rorya isipopita siku mbili, siku tatu lazima utakuta wananchi wameibiwa mifugo; na lengo kubwa la uanzishwaji wa Halmashauri zile mbili, mpaka ikafikia sehemu ikatengenezwa Polisi ili kuhudumia maeneo haya yote mawili, haipo sawasawa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ninavyozungumza, jana wananchi toka asubuhi mpaka saa 8.00 wanazunguka kutafuta mifugo yao ambayo imeibiwa. Uanzishwaji wa kanda maalum ndani ya ile Halmashauri kwa maana ya Tarime na Rorya, ilikuwa ni kuhakikisha angalau kuna usalama kwanza wa hizi Halmashauri mbili, lakini nisikufiche ningetamani sana Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani alichukulie serious suala hili, kwa sababu kule imekuwa ni kero kubwa sana. Leo Mheshimiwa Rais akienda au Waziri Mkuu, amini ninachokwambia, bango la kwanza atakalokutana nalo ni suala la wizi wa mfugo. Imekuwa ni suala la kihistoria, limekuwa la miaka mingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali kwa unyenyekevu mkubwa, watafute mbinu za kukomesha hili suala ili angalau wale wakazi wa Rorya ambao kimsingi wameamua kuhamasika kwenye kuingia kwenye shughuli za ufugaji, wafuge mifugo yao, kama ni ng’ombe ikiwa ni salama kabisa bila kuingiliana na huu msuguano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kwa sababu bila ya kufanyika, haya ndiyo yana mahusiano na mwingiliano wa ukuaji wa kiuchumi wa wananchi wangu. Kama utakutana na disturbance kwa maeneo haya mawili, maana yake kila mwaka watakuwa wanakwenda na bado watakuwa wanarudishwa nyuma, kwa sababu mtu anajikakamua, anaanza kufuga ng’ombe wawilia au watatu; na mwingine wale ng’ombe ndiyo anaotumia kulipa ada ya watoto wake. Mwingine wale ndiyo wanazitumia angalau akipata shida kuuza na kuingia kwenye shughuli zake za kiuchumi na kujiendesha katika maisha yake. Halafu haifiki mwisho, wale ng’ombe wanakuja kukwapuliwa, anaanza upya yule mwananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana sana, Wizara ya Mambo ya Ndani, kwa sababu nimeshafuatilia kwa muda mrefu, walichukue walione ni namna gani angalau wanalitatua ili wananchi nao waweze kujikwamua kwenye suala hilo la kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo machache, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nami niungane na mchangiaji aliyetoka kuchangia, kwanza kukushukuru wewe binafsi kwa sababu ni mara yangu ya kwanza kuzungumza katika Bunge hili na ni mara yangu ya kwanza wananchi wamenipa ridhaa ya kuongoza ndani ya Jimbo la Rorya, Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru wewe binafsi kwa namna ambavyo, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza nimeona namna unavyoliongoza Bunge, lakini imetupa faraja hasa Wabunge wengi wapya; kwa namna ambavyo tulikuwa tunakuona nje na hakika wewe ni kiongozi bora sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kabla sijasahau Mheshimiwa Spika, nianze kwa kuunga mkono hoja hotuba zote mbili za Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli; hotuba ya kwanza ilikuwa ya kufunga Bunge na ile aliyoitoa Novemba ya kufungua Bunge. Naunga mkono hoja hotuba hii.

Mheshimiwa Spika, nami niseme tu kwamba hotuba ya Rais wetu, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ilikuwa na mwelekeo chanya, ni hotuba ambayo ina matumaini mazuri kuanzia ngazi zote na sekta zote za kibiashara na kiuchumi na shughuli nyingi za ukuaji na ustawi wa jamii kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitaenda kuchangia kwenye baadhi ya maeneo ambayo nimeona angalau niweze kuchangia katika kuboresha na katika utekelezaji wake utakavyokuwa.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais wetu katika hotuba yake ukurasa wa 34 na 35 amezungumzia namna ambavyo Serikali yetu ya Jamhuri ya Muungano chini ya Chama chetu Cha Mapinduzi, ilifanya kazi kubwa sana katika uboreshaji na uinuaji wa sekta ya maji. Nichukue nafasi hii kwa moyo wa dhati sana kumshukuru Waziri mhusika wa Wizara hii. Naweza kusema, kwa muda mfupi wa miezi hii mitatu, mimi nimepata ridhaa ya kutembelewa na Waziri wa Maji. Kwa kweli nichukue nafasi hii kumpongeza kwa kazi kubwa aliyoifanya. Ni imani yangu alikuwa anatekeleza yale ambayo Mheshimiwa Rais amemwagiza na ndiyo haya ambayo wananchi wetu wanatarajia kuyaona.

Mheshimiwa Spika, jimbo langu kwa asilimia 77 limezungukwa na maji; asilimia 23 peke yake ndiyo eneo la nchi kavu ambalo wananchi wanalima na kufanya shughuli nyingine za kiuchumi. Kwa miaka yetu mitano kwa chama chetu na Mheshimiwa Rais wetu, alituletea zaidi ya shilingi bilioni saba kwa ajili ya uboreshaji wa huduma ya maji. Nilikuwa naiona hapa kwenye hotuba yake hapa ameisema, hizi shilingi trilioni 2.2 ambazo zimeletwa kuinua na kuboresha sekta ya maji, sisi katika Jimbo letu ni miongoni mwa Majimbo ambayo yamepokea fedha hizi, lakini niseme tu kwamba haikutumika vizuri.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri alipokuja kufanya ziara yake, ndiyo maana nimesema nianze kumpongeza, kuna maelekezo aliyatoa kutokana na namna fedha hizi zilivyotumika. Niendelee tu kumwomba Mheshimiwa Waziri aendelee kukazia hapo, kwa sababu ndani ya Jimbo langu, nina changamoto kubwa sana ya maji. Unaweza kuona hiyo asilima 77 ambayo inazungukwa na maji, lakini hatuna mradi mkubwa unaotokana na Ziwa Victoria, asilimia iliyobaki 23 ndiyo maeneo ya nchi kavu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais alitupa fedha ili angalau fedha hizi ziweze kuinua na kuwasaidia wananchi wanyonge hasa akina mama lakini haijatumika sawasawa. Nachukua nafasi hii kumwomba Mheshimiwa Waziri aendelee kukazia wakandarasi wote ambao walichukua hizi fedha za umma ili angalau waweze kurudi sasa kuweza kutimiza na kumalizia hii miradi.

Mheshimiwa Spika, unaweza ukakuta mkandarasi ametekeleza mradi kwa asilimia sitini lakini amelipwa asilimia mia moja na ameuacha ule mradi hauna maji. Amelipwa zaidi ya shilingi bilioni moja na ushee. Naomba Mheshimiwa Waziri aweze kukazia ili tuweze kulipata hili.

Mheshimiwa Spika, la pili, Mheshimiwa Rais katika hotuba yake amezungumza namna tulivyofanya kwa miaka yetu mitano na matarajio yake ya miaka mitano kwenye sekta ya afya. Mimi nishauri kidogo kwenye Wizara yetu hii ya Afya, ndani ya jimbo langu mimi nina vituo vinne tu vya afya lakini kiukweli kwa population na wingi wa watu ulivyo, vituo vya afya hivi havitoshi na unaweza ukakuta kituo kimoja cha afya kinahudumia zaidi ya vijiji 27. Kwa malengo mazuri ya Mheshimiwa Rais na naamini namna Waziri wa Afya anavyofanya kazi kwa muda toka amechaguliwa namwomba aitazame Rorya katika kipengele hiki cha upande wa sekta ya afya.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu unaweza ukakuta kituo kimoja cha afya kinahudumia zaidi ya vijiji 27, kina kata zaidi ya nane lakini ndani ya hicho kituo cha afya unakuta bado hakijapata huduma ya ambulance, wakati mwingine kuna changamoto kubwa sana kunapokuwa na wagonjwa kumtoa kwenye kata moja kumpeleka kwenye hospitali ya wilaya au kumsafirisha kwenda kwenye hospitali ya mkoa. Kwa hiyo, naomba na lenyewe hili ili kuendana na yale mazuri ambayo Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ameyazungumza kwenye hotuba yake tuyaboreshe sasa tuendane na kasi hiyo katika sekta hii ya afya.

Mheshimiwa Spika, la tatu, Mheshimiwa Rais amegusia vizuri sana upande wa barabara na sisi wote ni mashahidi kwa kazi kubwa iliyofanyika miaka mitano iliyopita. Tuna barabara ambayo imezungumzwa kwenye Ilani toka mwaka 2010, 2015, 2020, barabara ya kutoka Mika - Shirati, lakini inanyooka mpaka Kilongo kule mpakani. Barabara hii ina umuhimu wa aina mbili, moja ni barabara ambayo inainua uchumi ndani ya Jimbo letu la Rorya, lakini ni barabara ambayo kiusalama kwa sababu sisi tuko mpakani inaweza ikarahisisha shughuli za kiusalama ndani ya Jimbo kwa sababu ni sehemu ambayo tunapatikana kwenye mpaka wetu wa Kenya, Uganda pamoja na Tanzania.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue nafasi hii kumuomba Mheshimiwa Waziri husika, hii barabara kwa kipindi hiki ambacho imetajwa kwenye Ilani iingizwe kwenye utekelezaji angalau wa kupatiwa lami ili wananchi wa maeneo yale tuweze kuinua uchumi wao. Pili kama nilivyosema itakuwa ni sehemu nzuri sasa pia ya kuboresha upande wa ulinzi na usalama ndani ya jimbo.

Mheshimiwa Spika, nne, nizungumzie kidogo kuhusiana na TARURA. Pamoja na mambo mazuri na makubwa aliyofanya Mheshimiwa Rais, ndani ya Jimbo langu mimi la Rorya kuna shida kubwa sana ya barabara, hizi barabara za kuunganisha kata na kata na tarafa na tarafa ambapo ziko chini ya TARURA. Hivi navyozungumza kuna baadhi ya maeneo hayapitiki. Bado naamini kwa sababu ni mwanzo mzuri ambapo Serikali yetu ndiyo imeanza kufanya kazi chini ya Waziri Jafo, aone namna anavyoweza kutusaidia kwenye hii sekta hii ili angalau sasa tuendane na yale mazuri yaliyotajwa kwenye Ilani yetu hii na kwenye hotuba yetu ya Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli.

Mheshimiwa Spika, mwisho nizungumzie kuhusiana na wavuvi. Kwenye ukurasa wa 19, Mheshimiwa Rais amezungumza vizuri sana juu ya maboresho ya kodi na tozo mbalimbali zinazotolewa upande wa wenzetu wavuvi. Wabunge wote ambao wanatoka Kanda ya Ziwa watakuwa mashahidi, ilikuwa ni kazi kubwa sana kwa mwaka jana 2020 kupata kura kutoka kwa wananchi wanaofanya shughuli za uvuvi.

Mheshimiwa Spika, naomba kwa sababu Mheshimiwa Rais ametoa mwongozo mzuri sana kuhusiana na kupitia tozo zote ambazo zinawagusa wavuvi, Wizara kwanza ikae na hawa wavuvi wawape elimu na ipitie tozo hizo. Mimi nadhani si busara nzuri sana unapomkuta mvuvi anafanya biashara haramu ukamchomea mtumbwi wake kwa sababu wakati mwingine unakuta ule mtumbwi yeye mwenyewe siyo wa kwake, ameazima au amekodisha kutoka kwa mtu mwingine. Kwa hiyo, si tu kumrudisha yule mvuvi nyuma bali unamuathiri hata yule mmiliki halali wa ule mtumbwi.

Mheshimiwa Spika, wale wavuvi ndani ya jimbo na Kanda ya Ziwa wamekuwa wanalalamika kwa muda mrefu sana. Naiomba Wizara kipindi hiki turudi sasa tuone namna gani tunaweza tukapitia tozo lakini hata maboresho ya sheria ili angalau wale wenzetu wanaofanya shughuli za uvuvi wasiendelee kila siku kulalamika kwamba wanaonewa.

Mheshimiwa Spika, nikiri kwamba inawezekana wapo kweli wanaofanya biashara haramu na hawa sina maana kwamba tunatakiwa tuwatetee lakini wako ambao wananunua na wanapewa risiti halali kutoka kwenye maduka halali na wanakwenda kufanya biashara ile ya uvuvi. Mvuvi anakutwa ziwani ana risiti zote, ana mtego au ana nyenzo ile ile aliyonunua lakini wale watu wanamwambia kwamba wewe mtumbwi wako hauna uhalali wowote.

Mheshimiwa Spika, natamani sana Mheshimiwa Waziri kwenye kipengele hiki, maeneo yote ya Kanda ya Ziwa wakae wazungumze na hawa wavuvi na cha kwanza kabisa tutoe elimu. Kabla ya kumkamata uvuvi na kumpa kesi ya uhujumu uchumi, ningetamani sana tukae nao tuwaelimishe kwa sababu naamini mlinzi na mtetezi wa kwanza wa hizo maliasili ni mvuvi mwenyewe. Sisi Wabunge ambao tunatoka maeneo ya uvuvi, tuko tayari kutoa ushirikiano, wapewe elimu ili tuone namna gani tunanusuru hayo maeneo yote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nizungumze kidogo kuhusiana na rasilimali zetu. Moja kati ya kazi ya Mbunge ni pamoja na kutetea na kulinda maslahi ya wananchi na Serikali yetu kwa ujumla wake. Nilisema hili kwa sababu naamini Mheshimiwa Jafo ni mtendaji mzuri na anafanya kazi na anafuatilia sana utendaji na kulinda rasilimali za nchi.

Mheshimiwa Spika, kuna gari letu sisi ndani ya Halmashauri ya Rorya. Tulipewa gari hili na Serikali yetu kwa upendo kabisa toka mwaka 2009 lakini leo limekuwa na mkanganyiko mkubwa sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Jafari, Mbunge wa Rorya.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza kupitia kitabu cha Mpango tunaojadili wa mwaka mmoja na miaka mitano ukurasa wa 13; nipende tu kusema ndugu zangu Wabunge wote twende pamoja, pamoja na kwamba tunajadili Mpango ambao uko mbele yetu, tujaribu kukumbushana tu kupitia ukurasa wa 13 yale mazuri ambayo ameyafanya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ili tunapokwenda kujadili twende sambamba pasipo kupotosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, baadhi tu peke yake idadi ya kaya imeongezeka, zilizounganishiwa umeme zaidi ya 14.9% ndani ya miaka mitano (2015 mpaka 2020 Desemba). Vijiji vilivyounganishiwa umeme kutoka vijiji 2000 mpaka vijiji 10,000. Kuongezeka kwa kiwango cha uandikishaji, juzi Waheshimiwa Wabunge tulikuwa tunajadili hapa namna idadi ya wanafunzi walivyoongezeka mpaka madarasa yamepungua na mengine mengi ambayo ameyafanya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. Kwa hiyo tunapokwenda kujadili Mpango uliopo mbele yetu tunatakiwa tujadili yale mazuri ambayo yako mbele, lakini tujaribu kuainisha changamoto, namna gani sasa Waziri wa Mipango, Waziri aliyewasilisha Mpango huu aone namna gani sasa anatoka hapa ili kwenda mbele kuyafanyia kazi yale mawazo yote ya Waheshimiwa Wabunge bila kubagua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupitia hilo niende kujadili Jimbo langu la Rorya. Leo asubuhi tulikuwa tunajadili hapa Mheshimiwa Waziri alikuwa anajibu kuhusiana na hoja ya maji. Ndani ya Jimbo la Rorya, zaidi ya 77% imezungukwa na maji maana yake shughuli kubwa ya kiuchumi ukiacha shughuli ya kijamii ya maji, ni uvuvi. Mpango unasema kuna mradi mkubwa wa maji unaotekelezwa zaidi ya dola milioni 500 ambao unatoka kwenye Jimbo la Rorya unakwenda Tarime, lakini kijiji ambacho unatoka jimbo ambalo unatoka huo mradi halijawekwa kwenye mpango wa utekelezaji wa hayo maji. Kwa hiyo, naomba sana, tunapojadili na tunapopanga mipango tuangalie namna gani inagusa wananchi kwenye maeneo ambao mradi unatoka ili kwenda maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, ushauri wangu kwenye upande wa viwanda, natamani sana nimshauri Mheshimiwa Waziri upande wa viwanda, viwanda hivi ninavyovizungumza yawezekana visiwe vina mashiko sana hasa maeneo ya vijijini. Ningetamani sana Serikali ije na mpango wa namna gani ambayo itaanzisha viwanda ambavyo zinashiriki moja kwa moja kwenye shughuli za maendeleo za kiuchumi za kule ndani ya halmashauri, ikibidi waainishe mazao ya kibiashara ambayo yanatolewa kwenye halmashauri husika ili Serikali iwe na mpango wa kiwanda kulingana na zao la kibiashara linalozalishwa kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu ukitoa tathmini ongezeko la viwanda, leo tunasema kuna ongezeko la viwanda zaidi ya 8,400, yawezekana kwenye maeneo mengine hicho kiwanda hakipo. Kwa hiyo, yawezekana ukisema kuna ongezeko la viwanda kuna baadhi ya maeneo haliwagusi moja kwa moja wale wananchi, maana yake watakuwa wanashabikia ule mpango, lakini hauwagusi wale wananchi wa chini kabisa ambao tunawawakilisha. Ningetamani kwenye hii mipango Serikali izingatie sana unapopanga mipango ya kuongezeka viwanda, basi viwanda viwe moja kwa moja kwenye maeneo ambako kuna uzalishaji kwa wananchi hasa ukizingatia yale mazao wanayozalisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, nizungumzie sana upande wa uvuvi, mimi kama nilivyosema 77% ya jimbo langu inazungukwa na maji, shughuli kubwa inayofanyika kule ni uvuvi, lakini ndani ya miaka hii mitano iliyopita nyinyi wote mtakuwa mashahidi, wavuvi hawa hawana furaha kwenye maeneo yao. Ningetamani sana kama nilivyosema mara ya kwanza, Serikali ije na mpango wa namna gani itakaa na hawa wavuvi, ianishe na ione ni changamoto gani kubwa inawasumbua, kama shida ni nyenzo zile za uvuvi, wenyewe wanasema wanaponunua hakuna shida, ikija huku inakuwa na shida, Serikali ione namna gani inavyowasaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ningeomba Serikali kupitia Ofisi ya DPP iende ikaone wale wavuvi wadogo wadogo waliokamatwa kwa miaka mitano kwa makosa ya uhujumu uchumi ili iweze kuona namna gani inaweza ikawasaidia ili kuwaondoa, kwa sababu kuna wengine kimsingi mwingine hana hata fedha, lakini amekamatwa kwa makosa ya uhujumu uchumi. Kwa hiyo tuone namna gani kupitia Ofisi ya DPP inaweza ikawaona hawa watu na ikawasaidia kwa maana hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Muda umeisha Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kutoa maoni yangu kwenye mapendekezo ya mwongozo wa maandalizi ya mpango na bajeti ya Serikali na hatimae mapendekezo ya mpango wa maendeleo ya Taifa wa mwaka 2023/2024. Kwa sababu ya muda tu na kwa sababu ninayo mengi ambayo ningetamani na mimi nishauri ili yaweze kuingizwa kwenye utekelezaji wa mpango na hatimaye yaingizwe kwenye bajeti ili tutakapokuwa tunajadili mwakani basi mengi ambayo yanawagusa wananchi kwa ujumla wake Waziri wa Fedha pamoja na Serikali kwa ujumla wake, wawe wameyaweka kwenye bajeti ili angalao yalete ahueni kwa wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza mchango wangu nichukue nafasi hii kwanza kupitia kidogo taarifa ya Mheshimiwa Waziri kuhusiana na mtikisiko wa uchumi wa kidunia. Pamoja na mambo mengine ametaja sababu mbili ambazo ndiyo zinasababisha sasa mtikisiko wa kiuchumi kidunia, moja ni vita inayoendelea Ukraine, lakini la pili amezungumzia mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka tu nishauri kwenye hili la mabadiliko ya tabianchi ukisoma vizuri taarifa ya Mheshimiwa Waziri, niombe tu alipe mkazo kwa sababu, mabadiliko ya tabianchi sit u kwamba, yanakwenda kuathiri uchumi wa nchi, lakini pia yana madhara katika afya ya kibinadamu kwa ujumla wake. Kwa hiyo, nilikuwa natamani sana lipewe kipaumbele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanadamu tunaishi kutokana na ikolojia inayotuzunguka, lakini sote tunakubaliana kwamba, ikolojia ile imeanza kuathirika kutokana na shughili nyingi za kibinadamu, miti imeanza kukatwa na maeneo mengi sana yameanza kuathirika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu, hivi ninavyozungumza nchi wanachama wa Jumuiya ya Dunia wako Misri wanajadili juu ya mabadiliko ya tabianchi. Ningeomba sana Mheshimiwa Waziri uone namna ya kulijazilisha vizuri, namna ambavyo Serikali tumejipanga kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi kabla ya mwaka 2030 na kuendelea ili angalao isije ikafika huko tukakutana na changamozo hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema ya kwangu yatakuwa yale ambayo yanawagusa wananchi ambayo ningetamani yaingizwe kwenye bajeti. Kwanza, Mheshimiwa Waziri ningetamani sana bajeti ya mwakani pamoja na mpango wa bajeti hiyo ambao unakuja mwakani ili angalau tuweze kuujadili na kuupitisha, ni vema Wizara yako ingejipanga namna ya kuboresha na kuongeza mapato ya Halmashauri, hasa Halmashauri ambazo ziko pembezoni mwa mipaka ya nchi, lakini Halmashauri ambazo mapato yake yako chini ya bilioni moja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetamani mpango wako na bajeti ujikite sana tutakapokuja kujadili uone namna ambavyo unakwenda kuzisaidia hizi Halmashauri ili angalao zisiendelee kutegemea vyanzo vilevile kila mwaka. Mfano nitatoa, zipo Halmashauri ambazo zinategemea vyanzo viwili tu vya mapato. Ningeshauri sana kwenye Wizara yako kwa sababu huwa mnatenga fedha za miradi ya kimkakati na nimekuwa nilisema sana hili kwa Mheshimiwa Waziri. Muone hizi fedha za miradi ya kimkakati mpeleke kwenye Halmashauri ambazo mapato yake yako chini ya bilioni moja, lakini mapato yake hayako stable. Tungetamani kwenye bajeti ya mwakani inayokuja tupate angalao kujua fedha za miradi ya kimkakati zinazokwenda kwenye Halmashauri ambazo mapato yake hayako stable mnakwenda kuzisaidiaje? Kwa sababu, huko mbele haya mapato mwisho wake utafika yatakwisha, maana yake hizi Halmashauri hazitaweza kujiendesha. Kwa hiyo, ningetamani kwenye mpango na bajeti yako Mheshimiwa Waziri uone namna ya kulifanya hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kwenye mpango na bajeti tutakayokuja kuijadili mwakani, Mheshimiwa Waziri kwa sababu tunaishi na watu, ipo fedha ambayo inatolewa na Halmashauri ya asilimia 10 kwa ajili ya akinamama, vijana na watoto. Fedha hizi zinatolewa kulingana na kiasi ambacho Halmashauri zinakusanya. Zipo Halmashauri ambazo kiwango cha fedha wanachokusanya ni kidogo sana kiasi kwamba, kinachokwenda kwa vijana kwa ajili ya mikopo na akinamama hakitoshelezi. Ningetamani kupitia mpango wako uje utuambie nini mnajiandaa, hasa Halmashauri ambazo zinakusanya fedha kidogo kwa ujumla kwa vijana wa watu 10 unakuta mfano fedha wanayopewa ni Milioni Moja au Milioni Mbili ambayo haitoshi hata kujiendesha kwenye kikundi hicho ambacho kipo. Mnao mpango gani kama Wizara na Serikali kusaidia hizi Halmashauri ili fedha inayokwenda angalao kikundi kimoja kikipata fedha kiweze ku-sustain?

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili katika hilo ningetamani kwenye mpango na bajeti yako Mheshimiwa Waziri, ni vyema ukaona namna ya kupitia utaratibu na sheria za mfumo huu wote ambao unatoa fedha zinazokwenda kwenye miradi kwenye hivi vikundi vya vijana, akinamama na walemavu. Ningetamani mpango wako na bajeti hiyo ije iseme namna mlivyojipanga kama Serikali kupitia upya namna ya utoaji wa fedha, namna ya kupata vile vikundi, namna ya pesa zinavyopata kwa sababu, hawa ndiyo wananchi ambao wametuzunguka huko, hawa ndiyo wangetamani kwenye bajeti ya mwakani waone namna ambavyo inakwenda kushughulika na changamoto zao kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine katika hilo ningetamani kwenye mpango na bajeti yako Mheshimiwa Waziri utuambie ni namna gani mnakwenda kujenga kama Serikali, barabara za lami kwenye maeneo ambayo yanaunganisha kati ya nchi na nchi, kwenye maeneo ya miradi ya kimkakati ambayo kimsingi yanaweza yakainua uchumi wa nchi, pia kwenye Mkoa na Mkoa? Ningetamani kwenye bajeti yako pamoja na mapendekezo utakayokujanayo mwakani ili mtuambie kwenye Halmashuri ambazo kimsingi zinagusana nchi na nchi angalao wapate kidogo barabara za lami ili ku- sustain na kuibua uchumi wa nchi ile pamoja na zile Halmashauri na hatimaye ninyi kama Serikali naamini mtakuwa mmepata mapato mengi sana, ningetamani hilo pia Mheshimiwa Waziri uje utwambie ni namna gani ambavyo mmejipanga? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri katika hilo, uone namna ambavyo unaweza ukapitia Sheria za Manunuzi na utekelezaji wa maeneo mbalimbali. Sheria za Manunuzi ambazo ziko TARURA, RUWASA na maeneo mengine kwa sababu, naweza nikakutolea mfano Mheshimiwa Waziri; tumepitisha bajeti mwezi wa Saba, leo tunazungumza ni mwezi wa Novemba tunakwenda mwezi wa Disemba, bajeti ya fedha, fedha za mipango tulizopitisha kutekelezwa kuanzia mwezi wa Saba mpaka leo hakuna Mkandarasi site, hakuna kazi, maana yake ni nini? Hizi Taasisi zote bado zipo kwenye utaratibu wa kimanunuzi. Ningetamani kupitia ofisi yako upande wa fiscal policy au upande ambao wanahusika na mambo nya sera na sheria uone ni wapi ambapo tunakwama? Ni kwa nini tunapitisha bajeti mwezi Julai, lakini utekelezaji wake unakwenda zaidi ya miezi Minne katika utekelezaji wake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni kwamba, hata unaposema umeona kwenye bajeti yako wanasema angalao mwakani kuanzia Januari mpaka Juni, tunategemea uchumi wetu ukue kwa asilimia 5.3. Unaweza usikue kwa sababu, inawezekana mvua hizi zinazokuja barabara nyingi zitakuwa hazijatengenezwa. Hivi ninavyozungumza na wewe maeneo mengi umeme bado haujafika sawasawa, ninavyozungumza na wewe maeneo mengi bado miradi ya maji tuliyopitisha bajeti haijaanza kutekelezwa, hawa wote ukiwauliza ni utaratibu wa kimanunuzi ambao kimsingi ndiyo unasababisha hizi shughuli ziweze kuendelea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningetamani kwenye mpango na bajeti ili mje muone namna gani ambavyo mnaweza mkapitia, ili fedha inapotoka ya Serikali inakwenda moja kwa moja kwa mwananchi na isichukue muda mrefu na ikaleta maswali mengi sana kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ningetamani nilizungumze na tulilisema hapa Mheshimiwa Waziri na umelisema kwenye hotuba yako ni pamoja na usimamizi wa fedha mnazopeleka. Umesema kwenye hotuba yako kwamba, utaimarisha na kupeleka fedha kuimarisha simamizi hizi, ofisi ndogondogo za Ukaguzi za CAG ambazo ziko kwenye Halmashauri. Mimi nikuongezee lingine, pamoja na mipango yako na bajeti tafuta namna ambavyo utaongeza usimamizi kwa kuwalipa fedha Wasimamizi Wakuu wa fedha za miradi huko ni Madiwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwenye mpango na bajeti inayokuja mwakani ningetamani na penyewe uone namna hawa wasimamizi wa kwanza ambao leo unapeleka zaidi ya Bilioni Mbili kwenye Halmashauri kwa ajili ya ujenzi wa madarasa, msimamizi wa kwanza wa kuhakikisha fedha inatumika ni Diwani. Sasa lazima angalao kwa kuwa unaandaa fedha za kwenda kulipa namna ya usimamizi - CAG, angalia namna ambavyo unaweza ukaweka mpango mkakati mzuri wa kuwalipa wale Madiwani ili kazi zao ziweze kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri ni kuhusiana na ulinzi na usalama. Mimi niko kule Rorya na maeneo mengine, ningetamani sana kwenye mpango wa Serikali pamoja na bajeti muone namna ambavyo mnaweza mkapeleka fedha kwenye maeneo ya Maziwa na Bahari Kuu kuimarisha ulinzi na usalama wa maeneo yale. Niliwahi kutoa mfano hapa tunalinda sana maeneo ya maliasili na ndiyo maana tumeweka Jeshi Usu, ukienda kwenye madini kule wanalinda, lakini ukienda maeneo ya Maziwa na Baharini huku hakuna ulinzi wa rasilimali samaki na hakuna ulinzi wa wavuvi wanaovua maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikupe mfano na niliwahi kusema hapa, ukienda Rorya leo wavuvi kila siku wanalia kupigwa na kunyang’anywa nyavu zao, kupigwa na kunyang’anywa samaki, hakuna ulinzi. Kinachohitajika kule ni feasibility ya ulinzi angalao Askari waweze kuonekana, lakini hawapo. Nini ambacho ningeshauri katika hili kwenye maeneo ya Maziwa na Bahari, kwenye mpango wako na kwenye bajeti Mheshimiwa Waziri, uone namna unaweza kupeleka fedha kwa mfano maeneo ya Kanda ya Ziwa yote na Mkoa wa Mara ambao wanaathirika na hii shughuli ya kupigwa na kunyang’anywa samaki. Peleka fedha watu hawa waweze kununua mashine, ipo mashine pale Rorya ambayo ukubwa wake na utumiaji wa mafuta ni mkubwa sana kwa siku wanatumia zaidi ya lita 600 hawawezi Askari wale kuimarisha ulinzi maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamekuwa wakiiomba Serikali iweze kuwasaidia kupata mashine ndogo za watt power 40 mpaka 50 ili waweze kuratibu ulinzi wa maeneo yale ya Kanda ya Ziwa.

Mheshimiwa Spika, wavuvi wanapigwa sana, watu wanafilisika kule. Ningetamani kwenye ulinzi na usalama wa maeneo ya bahari Mheshimiwa Waziri nione namna mlivyojipanga kuimarisha rasilimali samaki kwenye maeneo ya maziwa ili angalao kuondokana na hili ambalo limekuwa likienda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo ningelisema hapa ni kuhusiana na kilimo. Nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo kwa namna anavyokwenda, lakini ningetamani pia hii block farming ambayo inaendelea ingeenda na kasi kwenye maeneo mengi ya nchi, pia iende sambamba na hili suala linalokwenda la utambuzi wa udongo ambao unafaa kwa aina fulani ya zao, hasa kwa Mikoa ambayo haina mazao ya kimkakati na mazao ya kibiashara, ikiwemo na Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili likienda haraka litatusaidia sisi kulingana na yale mabadiliko ya tabianchi ambayo kimsingi yanatuathiri maeneo mengi na ndiyo yanatusababishia baadae ukame na njaa, kutakuwa hakuna chakula. Block farming inaweza ikatusaidia hasa tukiendana na kilimo cha irrigation kwenye maeneo mengi kwa kutambua mazao ya kibiashara kwenye Mikoa ambayo haina, ili kukingana na kuepukana na hili linalokwenda. Ningetamani sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo na Mheshimiwa Waziri wa Fedha mtakapokuja kutenga fedha muendane kwanza na haya yote mliyoyapamga, lakini mwakani muende mtenge fedha kwenye Mikoa ambayo haina mazao ya miradi ya kimkakati ili kuweza kuimarisha na kuwapa fedha ili waweze kubuni, hasa Mkoa wa Mara ambao kimsingi umekuwa ukiathirika kwa kiwango kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie moja kama muda utakuwa unaniruhusu. Lipo suala la utekelezaji wa umeme wa REA na hapa tumekuwa tukijibiwa sana, mimi ningetamani sana kwa baadae kuna umuhimu wa kuja kupitia kanuni ya majibu ambayo kimsingi huwa yanatolewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utekelezaji wa umeme wa REA leo ninavyozungumza ambao kimsingi unakwamisha shughuli na bajeti tuliyopitisha, tusipolisema leo maana yake hata mwakani litakwamisha shughuli na bajeti tunayopitisha. Wakandarasi maeneo mengi hawako site au hawatekelezi, lakini Serikali imekuwa ikisema kufikia mwezi wa 12 tutamalizana na hili zoezi, haliwezekani Mheshimiwa Waziri. Mimi ningetamani kama linawezekana adhabu yoyote itolewe kwangu mimi itakapofika mwezi wa 12 kama Wakandarasi watakuwa wamemaliza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakupa mfano, Vijiji 13 Mkandarasi ametekeleza Kijiji kimoja tu ndiyo umeme unawaka, ana mwaka mmoja na nusu. Leo tumebakiza mwezi mmoja ukisimama ndani ya Bunge ukasema ndani ya mwezi mmoja utamaliza Vijiji 11 haileti maana. Mimi ninaomba sana fedha hizi za miradi, hizi ambazo zinachochea ukuaji wa uchumi kwenye umeme na maji zitoke kwa wakati, lakini usimamizi wake uweze kuwa imara sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2022
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa machangiaji wa kwanza. Ni-declare interest kwamba ni Mjumbe wa Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii. Kwa maana hiyo, naunga mkono mapendekezo yote ambayo yamesomwa mbele ya Bunge lako siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, natamani nikazie mambo kadhaa ambayo tumeyaweka kama maelekezo na maagizo, na mwishoni yatakuwa maazimio ya Bunge hili Tukufu. La kwanza ni zoezi hili la kuhamisha watu; wananchi walioridhia kuhama eneo la Ngorongoro kuhamia eneo la Msovela.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo mambo matatu ambayo tumeyaweka kwenye taarifa yetu. La kwanza ni Serikali kupitia Wizara ya Ardhi kuhakikisha inaharakisha kufuta GN ambazo kimsingi zinakwamisha uendelezaji na upangaji wa matumizi bora ya ardhi ya eneo la Msovela kwa ajili ya kuhakikisha wale wananchi wanaohamia pale hawapati usumbufu wowote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ni Serikali kuhakikisha angalau inatoa fedha kwenye kaya zaidi ya 1,500 ambazo zimeridhia kuhama. Ila sasa Wizara ya Maliasili na Utalii inapata changamoto hiyo kwa sababu ya upataikanaji wa fedha. Nichukue nafasi hii kuwashukuru; sina maana kwamba hawajafanya kazi, kwani wamefanya kazi kubwa na nzuri sana, lakini Serikali iharakishe ili kuona namna gani hawa wananchi ambao wameridhia kwa mapenzi yao wanahamia haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni maboresho ya sheria ya eneo la Ngorongoro ili angalau mwishoni tupate matumizi bora ya eneo lile kuondoka kwenye eneo la matumizi ya mseto na kuwa na matumizi ambayo ni sawa sawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne ni mradi wa Seven Eleven wa Kawe. Mradi huu ni wa Shirika la Nyumba; na kama tulivyosema kwenye Kamati, Serikali imekuwa ikipata hasara kubwa sana kupitia huu mradi. Kwa sasa umesimama na mkandarasi anadai zaidi ya Shilingi bilioni 44, hiyo ilikuwa ni mwezi Januari. Mpaka sasa ukienda deni ni zaidi ya Shilingi bilioni 54, na tunavyozidi kuchelewa kutatua mgogoro huu kila mwezi fedha hii inaongezeka. Tunatamani sana Serikali iingilie ione namna ya kuingilia mgogoro huu iweze kuumaliza na tusiendelee kupata hasara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la tano ni TANAPA. Mwaka 2019 TANAPA walikuwa na hifadhi wanazozisimia 16, lakini kuanzia 2016 tukaongeza hifadhi sita, sasa hivi wana hifadhi 22. Usimamizi wa hifadhi hizi ni mgumu sana, tulikuwa tunaomba angalau Serikali waweze kuongeza fedha ili watu hawa waweze kuendana na ongezeko hili la hifadhi ambalo tumeliongeza kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo hapa ambapo kimsingi natamani sana Bunge hili na Kiti chako kiweze kuweka msisitizo. Kuna jambo ambalo kimsingi linagusa maslahi ya Taifa hili. Nasi kama Kamati tumelileta ili angalau litoke kama azimio kwa ajili ya utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upo mradi wa uboreshaji wa usalama wa milki za ardhi ambao Serikali kwa maana ya kupitia Wizara tumepewa mkopo wa USD milioni 150. Kwa fedha ya Tanzania ni zaidi ya Shilingi bilioni 345, lakini lengo la fedha hizi lilikuwa: moja, ni kuimarisha usalama wa taarifa za ardhi; pili, ni kuimarisha miundombinu na upimaji; tatu, kujenga majengo ya ofisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi tunasema kupitia Kamati, tunadhani fedha hizi maeneo zilikopelekwa fedha hizi ambazo ni za mkopo, hazina tija moja kwa moja na mashiko kwenye maslahi mapana ya Taifa na wananchi na lengo kubwa la kutatua migogoro ya ardhi nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia Bunge hili, tunao Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano ambao kimsingi 2020 mpaka 2025 unasema tuwe tumepima asilimia 50, tuwe tumepanga matumizi ya vijiji angalau asilimia 50 ya vijiji vyote. Leo tuna vijiji zaidi ya 12,319 tumepanga matumizi vijiji 2,600 peke yake, maana yake hatuendani na kasi ya mpango. Vijiji 2,600 ni toka uhuru, lakini toka 2020 vijiji vilivyopangwa havizidi 200 peke yake, maana yake hatutakidhi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo Ilani ya Chama cha Mapinduzi, inazungumza hivyo hivyo kwamba mwaka 2020 mpaka 2025 tuwe tumepanga matumizi kwa asilimia 50. Tuna vijiji hivyo 2,640, tunayo hotuba ya Mheshimiwa Rais. Mwaka 2021 hapa, Mheshimiwa Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan alitoa maelekezo na dhamira yake ya Wizara hii kuhakikisha angalau inapanga matumizi bora ya ardhi katika maeneo mengi ili kutoa ukakasi na urasimu kwa wawekezaji wanaokuja kuwekeza ndani ya nchi. Yote hii inaendana na kasi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, ni Wabunge namna ambavyo tumekuwa tukichangia humu ndani ya Bunge. Migogoro mingi ya sekta ya ardhi inasababishwa na kutokuwa na mipango bora ya matumizi ya ardhi ngazi ya vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili liko wazi, kila Mbunge akisimama kuchangia humu ndani atakwambia namna mgogoro uliopo kati ya wakulima na wafugaji, namna mgogoro uliopo kati ya muwekezaji anayekuja kuwekeza na mwananchi, namna mgogoro uliopo kati ya mwananchi na mwananchi, namna mgogoro uliopo kati ya maeneo ya hifadhi na wananchi husika kwenye eneo husika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, solution ya kuondoa haya yote, ni kupanga matumizi bora ya ardhi katika maeneo yote. Sasa sisi toka uhuru tumepanga matumizi vijiji 2,640. Kamati inasema nini kwenye hili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa tumepata fedha zaidi ya Shilingi bilioni 345 na hapa wameelekeza kupanga matumizi vijiji 250 peke yake, Kamati inasema, kwa kuwa vijiji vilivyosalia 9,670 havijapangwa na havijaelekezwa mpango wa matumizi bora ya ardhi. Fedha hii ya mkopo ielekezwe zaidi ya asilimia 50 kupanga matumizi bora ya ardhi nchi nzima. Hii itakuwa ikakidhi haya manne niliyoyasema. Inakwenda kutekeleza mpango wa maendeleo, itatekeleza hotuba ya Mheshimiwa Rais, itatekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, na pia itakuwa inajibu yale maombi ya Bunge hili, namna bora ya kutatua migogoro ya nchi yote kwa ujumla wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ningeomba sana kwa msisitizo. Ukipiga vijiji 9,600 vilivyosalia, mpango wa matumizi bora kijiji kimoja ni Shilingi milioni 15 peke yake. Nilikuwa naangalia kwenye mkopo wetu tuliokopa sisi; Shilingi bilioni 345 unatakiwa utoe Shilingi bilioni 145 peke yake kwenda kutatua na kutengeneza historia ya nchi hii kwa kupanga matumizi bora nchi nzima. (Makofi)

Ndugu zangu Waheshimiwa Wabunge, hii ndiyo inaweza ikatutengenezea historia ya nchi hii kwa mara moja kupanga vijiji 9,600 kwa wakati mmoja. Kwa sababu toka uhuru tuna vijiji 2,600 peke yake, badala ya hizi fedha kuelekezwa kwenye maeneo ambayo kimsingi tukiyatazama hayana tija. Mfano, nitayasema maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi, ukichambua namna ambavyo Wizara maeneo ambayo inakwenda, ni fedha ya mkopo. Tunaelekeza fedha hizi mathalan kwenda kuandaa leseni za makazi zaidi ya milioni moja. Sipingani na hili, lakini tunakopa na tumeelekeza zaidi ya Shilingi bilioni 160 kwenye utekelezaji wa zoezi hili; tujiulize, leseni ya makazi ina-expire kwa miaka mitano peke yake. Taifa hili tumefikia mahali tunaelekeza mkopo wa Shilingi bilioni 160 kupeleka mahali ambapo baada ya miaka mitano ina-expire. Yaani baada ya miaka mitano, mnarudi kutafuta fedha nyingine kupanga eneo, fedha ya mkopo wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa natamani, kama tuna mpango wa kuboresha leseni za makazi, isitoke kwenye bajeti na isionekane fedha ya mkopo inakwenda maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tumeelekeza fedha hizi kutoa semina kwa watumishi zaidi ya Shilingi bilioni tano. Tumeelekeza fedha hizi, kufanya valuation ya rates ambazo ziko sokoni.

Ndugu zangu, anayetaka kununua kiwanja, rate ya square meter moja ya kiwanja au unataka kununua nyumba; square meter moja ya nyumba inakuwa determined na soko lenyewe linavyokutana kati ya mhitaji na mnunuzi. Hatuna sababu kama Serikali kukopa Shilingi bilioni tano kuelekeza kwenye maeneo ambayo rate yake inakuwa determined na soko husika. Yaani tunakopa fedha kupeleka Shilingi bilioni tano mahali ambapo tunaweza kutumia fedha za mradi kuelekeza kwenye maeneo hayo. Haileti tija yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tumekopa fedha, angalia kwenye huu mkopo, tunatenga contingency (fedha ya dharura) bilioni 17 kwa ajili ya kuja kulipa mkopo, hizi fedha zote ambazo naziainisha hapa tulikuwa tuna uwezo wa kuzipeleka na kukubaliana kama Bunge na kutoa maelekezo angalau Serikali iweze kupitia maeneo haya ya huu mkopo waende wakapange matumizi bora ya vijiji vyote nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hii nje tu ya kuondoa mgogoro, nje tu ya kwamba itakuwa imetatua mgogoro wa ardhi nchi nzima, lakini itakua; moja, imeongeza thamani ya ardhi maeneo yote nchi nzima; pili, kwa kutengeneza mpango bora wa matumizi ya ardhi, mwananchi mmojammoja atakwenda kunufaika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili kwa sababu tumelisema sisi na tumeliona kwamba lina ukakasi kidogo kwa namna maelekezo ya hii fedha inapokwenda, tunaomba Bunge hili kwenye maazimio tuishauri Serikali iweze kupitia upya mkopo huu na iende kwenye maeneo ambayo yana tija, iende kwenye maeneo ambayo yanamgusa mwananchi moja kwa moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo wananchi wetu kule wanapigana kati ya wakulima na wafugaji, wanaondolewa maeneo ya hifadhi. Kwa nini tusiende kupanga matumizi bora ya ardhi ya vijiji hivyo? Tunatengeneza historia leo kwa miaka mitano kuonekane tumepanga matumizi ya vijiji 9,600 wakati miaka 50 ya uhuru tumepanga…

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo sisi tumeshauri, tunaomba Bunge hili angalau muweze kuona ili fedha hii iende kwa maslahi mapana ya Taifa. Nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi nami kupata ridhaa ya kuchangia kwenye Wizara hii muhimu ambayo kimsingi inagusa Maisha ya wananchi wa chini, wananchi maskini kabisa wa maeneo yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema kwamba pamoja na yote hayo mahitaji ya mwananchi maskini, yule mwananchi wa chini kabisa mahitaji yake makubwa huwa ni barabara nzuri ya kumfanya atoke eneo moja kwenda eneo lingine, inamfanya awe na uhakika wa afya, Wizara hii inapoweka zahanati na kuweka kituo cha afya inamsaidia kumtengenezea yule mwananchi maskini mazingira mazuri ya kufika eneo husika, haya yote yanafanywa na Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii inapojenga madarasa, inaboresha miundombinu ya elimu inamsaidia mwananchi maskini kutoka eneo moja kwenda eneo lingine kwa muktadha huo, ndiyo maana nimesema leo nimepata bahati ya kuwasemea wananchi wanyonge kabisa ambao kimsingi kwa muktadha huo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuliona hilo akaamua kwa upendo mkubwa kupeleka fedha kwenye Wizara hii ili kufanya kazi kubwa kwa wananchi hawa maskini. Mheshimiwa Rais kipekee kabisa nimshukuru sana kwenye Jimbo langu la Rorya nilipokuja mwaka jana kuzungumza kuhusiana na daraja la Mto Mori ambalo linaunganisha Tarafa Tatu, nilizungumza kwa kuamini kwamba wale wananchi maskini wanaotakiwa kufanya shughuli za kibiashara kutoka eneo moja la Tarafa moja kwenda Tarafa nyingine kati ya Tarafa Nne, Tarafa Tatu zinakwenda kunufaika na daraja hili. Mheshimiwa Rais hakusita alinipa zaidi ya 1.5 billion, hivi ninavyozungumza daraja lile linajengwa eneo lile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kutambua mchango mkubwa na mchango mkubwa kwa wananchi maskini ameleta fedha kwa ajili ya miradi ya ujenzi wa madarasa nchi nzima ambao tunaziita UVIKO mimi sitamani tuziite UVIKO, Mimi kwangu nilipata zaidi ya Shilingi Bilioni 2.3, ni kwa sababu alitambua wananchi maskini wakati wanapofika kipindi cha kwenda mashuleni wanachangishwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa madarasa yale ili watoto wao waende kusoma, akaamua kumsaidia yule mwananchi wa chini kuleta fedha kwa ajili ya ujenzi wa madaraza hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais hakuishia hapo kwenye maeneo mengi kwa kutambua mchango mkubwa wa afya mwananchi maskini Mzee wa kawaida anapougua anahitaji apate huduma ya kwanza ni kupata dawa, akaona ili aweze kumboreshea mazingira hayo akaleta fedha kwenye Majimbo yote ya vituo vya afya pamoja na zahanati. Kwangu peke yake kwa mwaka mmoja wa Mheshimiwa Rais amenipa zaidi ya Shilingi Bilioni Moja kwa ajili ya ujenzi wa vituo vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nashawishika kusema kabisa hadharani kwamba Mheshimiwa Rais ameamua kushughulika na wananchi wa chini kabisa, hii ndiyo dhama na dhamira njema ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nirudi kuwashukuru Waheshimiwa Mawaziri kwa kutambua pamoja na kutuwakilisha vijana kwenye mchango na namna mnavyofanya kazi, sisi kama vijana hatuna budi kuwapongezeni na kuwashukuru kwa sababu kama kweli msingetimiza haya maana yake mlikuwa mnapoteza uaminifu mkubwa sana kwetu vijana, endeleeni kuchapa kazi kwa mchango huo mkiamini haya yote Mwenyezi Mungu atawajaalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo ninao ushauri wa aina mbili kwa Wizara hii, jambo la kwanza ni commitment yako kwenye Halmashauri, commitment hii uielekeze kwenye usimamizi wa fedha za miradi na hauwezi kuelekeza kwenye usimamizi wa fedha za miradi kama Waheshimiwa Madiwani hawako stable, kama Waheshimiwa Madiwani hawapati posho yao ya kueleweka ningetamani niungane na Waheshimiwa Wabunge wenzangu waliozungumza jana, badala ya kulipwa posho ya Shilingi 350,000 tuone namna gani Waheshimiwa Madiwani wenzetu wanalipwa mishahara badala ya kulipwa posho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni Mheshimiwa Waziri uimarishe sana usimamizi wa kufanyika vikao vya Madiwani. Mathalani kwangu vikao vya sasa vinavyofanyika leo ninapozungumza kinafanyika kikao cha Baraza la Madiwani kujadili robo ya pili ya mwaka wa bajeti, yaani toka mwezi wa Kumi Kikao cha Baraza la Madiwani hakijawahi kukaa kinakaa leo mwezi wa Nne. Sasa tazama hapo fedha zako za miradi nani anayesimamia, ni nani anaehoji?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati ya fedha iliyotakiwa ikae mwezi wa Februari, mwezi wa Januari, mwezi wa Disemba haijakaa inakaa mwezi wa Aprili kujadili mapato na matumizi ya fedha zilizokwenda hizi tunazungumza za Mama Samia za mwezi wa Desemba, Januari na Februari, ni nani anapeleka usimamizi ulio imara? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri ninakuomba ninajua na ninawaamini imarisheni commitment, wekeni commitment hasa kwa Wakurugenzi, vikao vya Madiwani vifanyike kwa wakati kwa sababu bila vikao vya Madiwani kufanyika kwa wakati maana yake hizi fedha zinazokwenda hazitapa usimamizi imara. Mheshimiwa Rais atakuwa anapeleka fedha, miradi inachelewa kuanza, na hakuna chochote kinachofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kwenye hili umetuletea fedha kwa ajili ya vituo vya afya na ninashukuru sana Mheshimiwa Rais ametuletea Milioni 500 kwenye Tarafa ambayo haikuwa na kituo cha afya. Watalaam wanakwenda wananchi wameshaamua wapi wanajenga kituo cha afya kwenye Kata husika, wanawaambiwa hairuhusiwi kujenga hapa tumepata mwongozo kutoka Wizarani. Wanazalisha mgogoro mwingine toka mwezi wa kwanza, wa pili, wa tatu, wa nne tunabaki kujadili wapi kiende kujengwa kituo cha afya ile fedha ya Mama Samia maana yake imekuja ndiyo maana tunasema fedha zinakuja za miradi lakini utekelezaji wake unachelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe Mheshimiwa Waziri commitment kwenye maeneo haya uweze kuweza kusimamiwa vizuri ili Wakurugenzi wasikuangushe mwisho wa siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili la ushauri kwenye fedha ya miradi ya kimkakati. Mheshimiwa Waziri ni lazima fedha za miradi ya mkakati ziende kwenye Halmashauri ambazo hazina mapato stable, mapato yake hayapo stable mathalani kwangu Rorya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili niweze kuendesha Halmashauri mapato yangu yanategemea aina tatu, moja ni uvuvi, mbili ni kilimo, tatu ni ufugaji. Sasa ninyi Waheshimiwa Wabunge na Mheshimiwa Waziri wewe unafahamu kwa miaka mitatu hii mfululizo mpaka leo namna ya uvuvi wa nchi hii ulivyoathirika, kuna watu wamefilisika, kuna watu wamekimbia kwenye sekta ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Halmashauri fedha inayokusanywa kwenye uvuvi ni ya wale wavuvi wadogo ambao inasubiri wakavue irudi kupanga mipango mikakati ya maendeleo. Ukienda kwenye kilimo hatuna irrigation scheme yoyote inayofanyika ndani ya Wilaya ile, maana yake anasubiri mkulima mdogo alime mazao yake, akiwa anapeleka kwenye minada ikachukua ushuru ipange miradi ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuende kwenye ufugaji, leo tunafanya ufugaji ambao ili mwananchi aweze kupeleka mfugo wake kwenye mnada Halmashauri iende ikachukue kodi ichukue fedha ipange miradi ya kimaendeleo. Hatuna mradi mkubwa zaidi ya hii miradi ya kimaendeleo ya ujenzi wa vituo vya afya ambao unazidi Bilioni Moja au Milioni 500 ambao unaweza ku-sustain ukuaji wa uchumi wa Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba kwenye fedha za miradi ya kimkakati, kwa kuwa tayari nimeona imepangwa bajeti peleka fedha kwenye hizi Halmashauri ambazo mapato yake ya Halmashauri hayapo-stable ambayo ukitazama kwa namna muda unavyokwenda itafika mahali hizi halmashauri zita collapse.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu kama uvuvi unakwenda na umeshuka kweli kweli lini Halmashauri baada ya miaka mitatu, minne, mitano huko mbeleni itaweza kujiendeshaje.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuleta ombi Mheshimiwa Waziri kutumia fursa ya kwetu sisi ya kimpaka kule Kirongwe. Wilaya yetu imepakana na nchi ya Kenya tukaleta hapa maombi na nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, kwa kulitambua akaamua kutupa fedha kwa ajili ya kujenga one border post - Kirongwe ili tutumie fursa ya kimpaka wa Kenya na Tanzania, lakini kujenga one border post bila kuwa na fedha za kimkakati za kujenga soko pale haitatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe kupitia fedha zako za kimkakati kupitia kuisaidia na kuinusuru ile Halmashauri utupe fedha ili tuweze kujenga soko la kisasa pale mpakani ili tuweze kunufaika na soko la Kenya na Tanzania kwa sababu tayari Wizara ya ardhi imekwishatupa fedha kwa ajili ya kujenga one border post, utakuwa umetusaidia sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia utupe fedha ya mradi ya kimkakati kwa ajili ya ujenzi wa stendi ya Mika. Ndugu yangu Mheshimiwa Waziri unapoingia daraja la Kirumi pale mpaka unakwenda Tarime ile yote ni Rorya lakini wewe ni shahidi hakuna stendi yoyote ambayo magari yanaingia kwa ajili ya kulipa ushuru na hakuna stendi yoyote ambayo wananchi wanafaidika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe kwenye eneo lile kwenye fedha za miradi ya kimkakati nipe fedha angalau tuweze kuweka stendi na soko pale ili tuweze kusaidia vyanzo hivi ambavyo havipo imara vya Halmashauri vya kila mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunayo maeneo mengine mengi tu, tuna eneo la Nyanchabakenye pale ukitupa fedha kwenye ujenzi wa stendi bado ninaweza nika- sustain na kuendesha maeneo yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nizungumzie kuhusiana na maeneo ya miradi hii. Tunayo maeneo ambayo Mheshimiwa Waziri yanaunganisha kati ya Kata na Kata, naomba tupate fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja la Nyathorogo ambalo linatuunganisha kati ya Kata ya Nyathorogo na Kata ya Tarime vijijini kwa sababu bila kufanya hivyo wananchi wa eneo moja hawawezi kutoka eneo moja kwenda eneo la pili. Ninaomba nipate fedha kwa ajili ya ujenzi wa daraja linalouunganisha Kata mbili Kata ya Kitembe na Kata ya Roche ili angalau kuweza kuwasaidia wananchi wanaotoka eneo la Kata moja na Kata nyingine. Kwa kufanya hivyo kama nilivyotangulia kusema unakuwa umemsaidia na umemkomboa mwananchi maskini ambaye kimsingi anakuwa amelima mazao yake anataka atafute soko la upande wa pili lakini hana namna ya kufika eneo la upande wa pili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nikuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu tumeziweka kwenye fedha za miradi ya kimaendeleo utusaidie sana, lakini pale utakapoweza Mheshimiwa Waziri tusaidie pia kutokana na jiografia ya Jimbo la Rorya niliwahi kusema hapa, vituo vya afya vya maeneo ya mpakani mwa Kenya tunazo Kata zaidi ya tatu zinapakana na Kenya hazina kituo cha afya ambacho ni imara. Ninakuomba Mheshimiwa Waziri angalia Kata ya Roche, Kata ya Goribe na Kata ya Bukura kama wanaweza sehemu mojawapo kupata kituo kizuri cha afya, Kata hizi zote tatu zinapakana na nchi ya Kenya lakini wananchi wa mpakani hawa hawana namna ya kupata kituo cha afya maeneo yale, hawana huduma hiyo. Kwa hiyo nikuombe maeneo haya kupitia zile Kata za kimkakati tupate kituo maeneo yale ili kuboresha na kudumisha maeneo yale ya kiuchumi ili angalau wale wananchi wanapopata shida kwenye sekta ya afya waweze kupata mahali pengine pa kuweza kupata matibabu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikuombe la mwisho, kupata fedha za miradi ya dharura zipo barabara ambazo nimeziwakilisha kwa Mkurugenzi wa TARURA. Tuna barabara moja ya kutoka Shirati kwenda Minigo hii barabara hivi tunavyozungumza haipitiki kutokana na mvua zilivyonyesha. Tuna barabara moja ya kwenda Kuruya kwenda Marasibora, Randa kwenda Masike, Masangura kwenda Koryo, Nyamusi kwenda Panyakoo pamoja na Shirati. Barabara hizi ninavyozungumza Mheshimiwa Waziri hazipitiki na kwa sababu tumekwishaleta maombi ya fedha ya dharura ili angalau kwa kipindi hiki mvua inavyonyesha wananchi wetu waweze kutoka eneo moja kwenda eneo lingine. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri niweze kupata fedha kwa ajili ya uboreshaji huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya haya machache nakushukuru sana naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maji
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru. Japo niliomba kuchangia kesho, lakini kwa sababu ya tayari umeshanipa ridhaa hii nami niwe miongoni mwa wachangiaji ambao wamechangia Wizara hii ya Maji, Wizara nyeti kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru nitachangia maeneo matatu, la kwanza nitaanza na shukrani kubwa kwa Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa ujumla, lakini la pili nitakuwa na maombi, la tatu nitatoa shukrani kubwa kwa Wizara kwa mambo makubwa waliyoyafanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kusema kama wenzangu walivyotangulia kumshukuru Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wake wote kwa kazi kubwa, nzuri waliyoifanya, lakini nimshukuru mama Samia Suluhu Hassan, Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa maana ya kwamba, bila yeye naamini kabisa nguvu ya Mheshimiwa Waziri ingekuwa hapa na sisi tusingepata kutoa pongezi kubwa ambazo leo tunazitoa kwa Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakupongeza Mheshimiwa Waziri kwa mambo makuu matatu, la kwanza ni kwa namna ulivyo mnyenyekevu kuwasikiliza Waheshimiwa Wabunge wanapokuja kwako na changamoto, namna unavyojishusha, hata pale ambapo hauna fedha unajua sina namna ya kutekeleza hili Mheshimiwa Mbunge analoniambia, lakini wewe unalibeba kuonesha kwamba, tayari una uwezo na kumpa matumaini Mheshimiwa Mbunge aliyekuja kwako, hili ndilo linalokubeba kwa asilimia kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni namna ambavyo unaonekana kwenye dhamira ya dhati ya kutatua changamoto kubwa yam aji nchi hii. Hili nakuona kabisa pale unapozungumza na hata mtu anapokutana na wewe namna unavyojipambanua kuonesha kweli dhamira yako kuanzia uso, maneno unayoyazungumza na vitendo vyako ambavyo umedhamiria. Hili linakupa sifa kubwa sana kwenye pongezi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu nikupongeze kwa namna ambavyo nilivyokuja kwako baada ya uchaguzi, 2020 baada ya miezi mitatu tu. Nilikuja na changamoto kadhaa kwenye wilaya yangu, pale Shirati leo hii wanakuita mkwe, wanakuita kwa sababu walikuwa wana zaidi ya miaka 10 wanaomba huduma yam aji pale, kumi-kumi na mitano, baada ya uchaguzi ule Mheshimiwa Waziri uliniahidi ndani ya siku 100 eneo lile lote la Kata ile ya Mkoma wanapata maji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na kweli ndani ya miezi mitatu Mheshimiwa Waziri nikupongeze kwa kiasi kikubwa kwa sababu, baada ya miezi mitatu wananchi wa pale Shiratu walipata maji safi na salama na leo hii umenitengenezea jina, lakini umetengenezea jina Chama Cha Mapinduzi kwa ujumla wake hasa ukizingatia kata ile miaka yote ilikuwa ni kata ya upinzani. Leo tunazungumza kwa kazi kubwa uliyoifanya wale wananchi hawana namna wanakupongeza na wanakushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio huo mradi peke yake, kuna miradi kongwe ambayo ilikuwa imesimama ndani ya wilaya ile, kuna mradi wa Nyarombo. Mheshimiwa Waziri mradi ule ni zaidi ya miaka mitano na kuendelea, umekuja kwenye utendaji wako unafanya kazi. Mradi wa Kiamuameko Muge hivi ninavyokwambia unatoa maji. Mradi wa Roche zaidi ya miaka mitano huko nyuma, ninavyozungumza sasa hivi unatoa maji. Mradi wa Marasibora, mradi ambao ulikuwa ni kichefuchefu katika miradi uliyoitaja, leo ninavyozungumza na wewe unatoa maji. Mradi wa Nyambori ambao ulikuwa kimsingi yote hii ni miradi ambayo Mheshimiwa Waziri kwa namna unavyofanya kazi ninavyozungumza na wewe ndio maana nikasema ni lazima nikushukuru kwa kazi kubwa nzuri unayoifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile nikushukuru Mheshimiwa Waziri katika utendaji wako ukiacha hii miradi ya nyuma, umenipa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi, mfano fedha ya Uvico. Leo ninavyozungumza tunatekeleza mradi wa maji kwa fedha ya Uvico kutoka Shirati unakwenda Kata ya Raranya mpaka Ingrijuu kule. Mheshimiwa Waziri sina namna ya kukupongeza na kukushukuru kwa kazi kubwa nzuri unayoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kukushukuru wewe na kukupongeza nichukue nafasi hii kumpongeza na kumshukuru sana meneja wa wilaya yangu ya Rorya, Engineer James, ni kijana ambaye umeniletea baada ya kumuondoa yule aliyekuwepo na uliniahidi kwamba nakuletea kijana ambaye atafanya kazi nzuri sana. Mheshimiwa Waziri nikuombe utafute namna hawa vijana ngazi za wilaya wanaofanya kazi vizuri muone namna ambavyo mnaweza kuwapa promotion, ili waendelee kuwa na moyo wa kutekeleza yale ambayo Serikali imekusudia kuyafanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri nikushukuru sana. Naendelea kukushukuru kwa fedha ulizonipa kwenye mradi wa Kata ya Rabol katika vijiji vyake vyote vitano. Nikushukuru kwa fedha ulizonipa kwenye mradi wa Gabimoori kule Nyamagaro na mengine mengi Mheshimiwa Waziri umekuwa ukiyafanya. Pamoja na uzuri wa haya Mheshimiwa Waziri, nilivyoingia kwa status iliyokuwepo niliwahi kukwambia, wilaya yangu ndio wilaya inayozungukwa na maji kwa asilimia kubwa Mkoa wa Mara, zaidi ya asilimia 77 inazungukwa, asalimia 23 peke yake ndio nchi kavu ambayo utafanya shughuli za kijamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nakwambia leo inawezekana ukizunguka kwenye Mkoa wa Mara pamoja na haya mazuri uliyoyafanya inawezekana ndio wilaya yenye changamoto kubwa sana ya maji kuliko wilaya nyingine zote. Na nikakwambia kipindi tunaingia ni vijiji 12 peke yake kwenye wilaya katika vijiji 87 ndani ya wilaya vilivyokuwa vina maji, vijiji 25 vilikuwa vina miradi ambayo inaendelea, vijiji zaidi ya 50 havikuwa na mradi wowote wa maji katika utekelezaji wake, lakini nakushukuru angalao katika miradi hiyo ulivyoingia na hii niliyoisema hapa angalau leo tunazungumza zaidi ya vijiji 35 vina maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu ni nini Mheshimiwa Waziri; tunayo miradi miwili mikubwa ambayo ninaamini kabisa ukiweka fedha pale ninaamini kabisa utatusaidia kwa kiasi kikubwa. Mradi wa kwanza ni huu mradi wa miji 28. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri kama ulivyotuahidi bajeti yam waka jana na saa hizi umesema tena hapa, pamoja na iliyokuwa inazungumzwa kwamba, miradi ile haitatekelezwa, nikuombe kwenye miradi ya miji 28 utuondolee hii aibu ambayo ipo ndani ya wilaya kwamba, tunazungukwa zaidi ya asilimia 77, maji sisi wengine wamezungumza hapa ni kilometa mia mbili na kwenda juu, sisi Mheshimiwa Waziri ndani ya mita mia mbili, ndani ya mita mia moja, kuna wengine ndani ya mita hamsini tunayaona yale maji, lakini hatuna maji safi na salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni aibu iliyoje kwa Mheshimiwa Mbunge kwa miaka nenda-rudi unakwenda kwenye maeneo yale unazungumzia maji ambayo wananchi wanayaoga, lakini hawana maji safi na salama. Nikuombe kupitia mradi wa miji 28 nafikiri wewe unafahamu na kwa sababu, umefika kule zaidi ya mara mbili tuondolee hii aibu kututekelezea kwenye ule mradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna mradi wa vijiji ambavyo vilikuwa vinatekelezwa, vile ambavyo vinazungukwa na Ziwa Viktoria. Kwangu nina vijiji zaidi ya 20 ukiangalia kwenye ile takwimu, ukitekeleza haya mawili, vijiji ambavyo vinazungukwa na Ziwa Viktoria vijiji 20, ukatekeleza ile miji 28 ndani ya wilaya yangu utakuwa umeondoa asilimia kubwa sana ya upungufu wa maji. Na nikuombe Mheshimiwa Waziri katika hili tuachane na ule utaratibu wa kuzungumzia asilimia katika utekelezaji wa maji twende tuangalie namna ya kutaja vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mimi leo nikikwambia nina vijiji 87, vijiji vyenye maji ni 35, vijiji vilivyosalia zaidi ya 42 havina maji, hiyo ndio takwimu unayotakiwa Kwenda nayo. Ukienda na takwimu ya asilimia wakati mwingine yanachukuliwa maji yale ambayo yanaenda na msimu wa mvua. Tukisema hiyo asilimia ya utekelezaji wa maji kutokana na msimu wa mvua ile inatuchanganya kwenye rekodi zetu. Twende kwenye utekelezaji wa vijiji na kwa sababu umekwishafanya kazi kubwa sana uone vijiji vyote ambavyo tayari umefikisha maji vingapi havina maji na uende mpaka ngazi ya vitongoji usiishie kwenye vijiji peke yake kwa sababu, Kijiji kimoja kinaweza kikawa na vitongoji vinne, lakini maji yapo kwenye kitongoji kimoja. Ukienda kwa hiyo, status itakuwa ni rahisi sasa kujua na mipango yako ya mbele namna gani kwa kiasi kilichobakia uweze kukitekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie niende kwenye maombi yangu mengine sambamba na hili. Kuna miradi ambayo Mheshimiwa Waziri ulivyokuja kufanya ziara ilikuwa inatakiwa itoe maji, kwa mfano Mradi wa Komuge. Nikushukuru kwa kiwango ambacho imekeishafanyika, lakini nikuombe kwa sababu, kuna fedha ambayo iliombwa kwenye bajeti huu unakwenda mwezi wa sita, wape fedha wale vijana ili waweze kutekeleza yale maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi mwingine wa Nyehara, Kijiji kile ambacho nilikwambia, Kata ya Chang’ombe. Wape fedha ili waweze kutekeleza ule mradi angalao tuweze kufika mahali na sisi tukasema tunajivunia yale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nikushukuru sana, la mwisho, nitoe shukrani sana kwa namna ambavyo nimeona vijiji umeviweka vinakwenda kutekelezwa kwenye bajeti ya mwaka huu. Kijiji… kinakwenda kutekelezwa kwenye bajeti ya mwaka huu, Bubumbi, Sota, Sakawa, Kabache, Roche, Osiri, Kwatia, Kirong’we, Mang’ore, Kyogo, kwa maana ya upanuzi wake. Chereche, Deti, Ochuna, Omuga, Orio pamoja na Makongoro. Mheshimiwa Waziri nikuombe hivi vijiji ambavyo nimetaja vimetengewa fedha, fedha ikienda naamini itafika itasaidia asilimia kubwa wilaya yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana, pamoja na kwamba, umenishtukiza, lakini nimetoa mchango wangu. Nakushukuru sana, ahsante sana. Naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami nishiriki na Wabunge wenzangu kuanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu, Mama Samia Suluhu Hassan kwa kuhakikisha anatupatia fedha nyingi za miradi ya maendeleo. Sisi Wabunge kama Wabunge pamoja na Madiwani na wananchi kwa ujumla angalau sasa tunasimama kifua mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru sana Mheshimiwa Waziri pamoja na watendaji wote wa TAMISEMI kwa kazi kubwa wanayoifanya kusimamia fedha hizi na kuhakikisha angalau yale makusudio na matamanio ya wananchi ya Mheshimiwa Rais yanafikiwa kwa wakati wake. Nachukua nafasi kukushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa fedha ulizonipa hasa kwenye upande wa elimu na TARURA. Mwezi uliopita nilikuwa naadhimisha uzinduzi wa madaraja ya kihistoria ndani ya Wilaya yangu, ni kwa sababu ya utendaji mzuri wa Mheshimiwa Rais, pia na Wizara ya TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu walionitangulia kukuomba Mheshimiwa Waziri uone namna ya kuongeza fedha kwa watu wa TARURA hasa kwenye miradi ya kimaendeleo. Fedha hizi Mheshimiwa Waziri, TARURA ndiyo msingi wa kila kitu kwa wananchi, inatusaidia kutuunganisha kati ya Kijiji na Kijiji, Kata na Kata, na pia inasaidia sana wananchi wanyonge pale wanapotaka kusafirisha na kufanya shughuli zao za kiuchumi. Naomba ulione hili na namna ya kuwaongezea fedha hasa kwenye miradi ya kimaendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia hapa Mheshimiwa Waziri, kwangu kwa Mkoa wa Mara wote ukiacha Wilaya ya Rorya tu peke yake, sijaona fedha yoyote iliyotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo kwa upande wa TARURA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninayo madaraja mawili pale yanaunganisha kati ya Kata na Kata kwa maana Nyakorogo, kuna Komaswa na pia inaunganisha Kata ya Kigunga na Kata ya Nyaburongo. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri, haya madaraja mawili tuliyoyaomba sisi watu wa TARURA, na watu wa TARURA tukayaweka kwenye file la miradi ya kimaendeleo, unipe fedha ili niweze kutimiza haya madaraja mwishoni niunganishe na yale madaraja ambayo umeshanipa fedha ili tuweze kutekeleza yale ambayo yanatakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais anatimiza wajibu wake. Kazi yetu sisi kama Wabunge, viongozi wa kisiasa pamoja na watumishi, katika wajibu wa Mheshimiwa Rais wa kupeleka fedha ni kuhakikisha fedha inapokwenda kwenye miradi inasimamiwa ipasavyo na inazaa matunda. Tutakuwa Bunge ambalo halitakuwa lina matunda mazuri kama itakuwa kila tukisimama tunamsifia Mheshimiwa Rais kwa kupeleka fedha, lakini kule inapokwenda, usimamizi wa miradi ya maendeleo; moja, haikamiliki lakini mbili, inapigwa na inaliwa hadharani na watumishi ambao kimsingi wameamua kutoendana na kasi ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana kupitia Bunge hili kama viongozi wa kisiasa, pamoja na kusifia fedha nyingi zinazopelekwa na Mheshimiwa Rais, tutimize wajibu wetu kwa kuhakikisha angalau zile fdha zinazaa matunda. Kabla hata ya kusubiri taarifa ya CAG, Sisi tuwe ni watu wa kwanza kuhakikisha zile fedha angalau zinazaa matunda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi Profesa, Mbunge wa Kahama, alisema neno zuri sana. Mbwa mzuri ni yule anayebweka kabla mwizi hajaiba, lakini mbwa ambaye anabweka baada ya mwizi kuwa ameiba, yule anakuwa sio mbwa. Kwa kifupi ni kama wale mbwa tunaowaita mbwa koko. Sisi hatutaki kwenda kwenye masuala ya mbwa, tunataka twende kwenye udhibiti wa fedha za umma zinavyokwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano. Mheshimiwa Waziri unisikilize vizuri. Tunayo Hospitali ya Wilaya pale, imejengwa toka mwaka 2017. Awamu zote hizi, fedha imekuwa ikienda tumepelekewa jumla ya zaidi ya Shilingi bilioni 3.1 kwa ajili ya kujenga majengo 14 na ile Hospitali iweze kufanya kazi. Mheshimiwa Rais, Mama Samia kwa awamu yake peke yake, ametupatia shilingi milioni 500 na akatupatia tena shilingi milioni 800 kwa nia njema kabisa kuhakikisha yale majengo yanakamilika na yanawasaidia wananchi. Leo ninavyozungumza na wewe, majengo yote 14 hakuna jengo hata moja lililokamilika kwa ajili ya kutoa huduma kwa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukajiuliza, hizi fedha zinakwenda kwa ajili ya kutimiza, na hii ni bajeti ambayo inapangwa kwenye maeneo mengine ya Halmashauri nyingine; kwa nini Halmashauri nyingine wakipewa shilingi milioni 500 wana uwezo wa kukamilisha majengo matatu, lakini Wilaya ya Rorya haiwezi kukamilisha majengo hayo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hili Mhehsimiwa Waziri alitizame kwa jicho la upana. Umemsikia Mbunge Mheshimiwa Getere anazungumza hapa; ukimsikiliza Mkuu wa Mkoa na nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mkuu wa Mkoa wa Mara, toka amefika ni miongoni wa Wakuu wa Mkoa ambao wamekuwa wakisema miradi ya maendeleo kwa Mkoa mzima wa Mara haikamiliki. Fedha zinakuja lakini hazikamilishi miradi. Moja ni hiyo Hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nachukua nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Naibu Waziri, alikuja akaona. Katika sehemu ambazo zina vichekesho ukifika Mkoa wa Mara, ni Hospitali ya Wilaya ya Rorya. Inakuja fedha, shilingi milioni 500 ya kujenga madarasa matatu, mtu hajaanza kuchimba msingi, amenunua bati, na ananunua bati over estimation inayotakiwa. Kama bati zinatakiwa 100, anaomba bati 200. Anajenga shilingi milioni 500 inakuja; unamletea shilingi milioni 800, vile vilivyobaki stoo, hahami navyo kwenda kujenga kwenye miradi mingine, anakwenda kununua kwingine ili kupata 10%. Vitu vinabaki stoo, vinaharibika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba mpaka mwisho fedha zinakwenda, miradi haikamiliki. Tunasubiri taarifa ya CAG ili aje aseme, ndiyo tuanze kuzungumza ndani ya Bunge wakati tuna uwezo wa kwenda na kudhibiti na kuchukua hatua kwa mtu yeyote ambaye anaharibu na anaharibu jina la Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nakuomba sana Mheshimiwa Waziri na nimekuwa nikikuomba sana, kwanza ufanye ziara ya kutembelea Hospitali ya Wilaya ili uweze kuona haya yanayofanyika pale, kwa nini Hospitali za Wilaya hazifanyi kazi? Kwa nini tumepewa zaidi ya shilingi bilioni tatu, maeneo mengine Hospitali za Wilaya zimezinduliwa, kwa nini Mkoa wa Mara na Rorya Hospitali hizi hazifanyi kazi? Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri hili aweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili kwenye kichekesho hicho hicho, sisi tulikaa na Baraza la Madiwani. Tumeanzia Kamati ya Fedha, tumekaa Baraza la Madiwani, tumepitisha Bajeti ya makadirio na makusanyo ya mapato ya ndani. Sisi ndio tumedhamiria kwamba kiasi hiki tunakusanya kama fedha za mapato ya ndani. Tumejiwekea shilingi bilioni 1.7, inakuja huku kwenu, inapunguzwa, mnasema hawawezi kukusanya 1.7, wakusanye 1.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiuliza, kwa hiyo, tunamfurahisha nani? Kama sisi tumefanya tathmini ya Baraza la Madiwani ambalo liko kikanuni na kisheria, limepitisha shilingi bilioni 1.7 ambayo tutakusanya kwa mwaka, na ninyi ndio mnawaambia Baraza la Madiwani wasimamie mapato na matumizi na mianya inayopoteza mapato; wameazimia kwamba sisi tunataka tu tukusanye shilingi bilioni 1.7, inakuja huku mnasema, hapana, tunawawekea shilingi bilioni 1.5. Nimeona hapa mnatuwekea shiligi bilioni 1.5 ya mapato ya ndani. Najiuliza, hii mmeitoa wapi? Inatoka wapi kama Baraza la Madiwani lenyewe limekaa na wataalamu, wamedhamiria kukusanya shilingi bilioni 1.7? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa madhara yake ni nini? Mwishoni ndiyo mnakuja kutuweka kwenye asilimia 20 ambayo alikuwa anaizungumza Mbunge mmoja hapa, kwamba fedha ya maendeleo itaenda asilimia 10, fedha ya mikopo ya vijana itaenda asilimia 10. Mmetutoa kwenye asilimia 40, mmetupunguzia fedha ya mapato yetu na kuwa madogo na wakati sisi mapato yetu tumeweka shilingi bilioni 1.7, ninyi mmeshusha, mmeweka shilingi bilioni 1.5.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwaomba Mheshimiwa Waziri, kwanza, irudi shilingi bilioni 1.7 kama ilivyopitishwa na kikao halali cha Baraza la Madiwani, na pili asilimia 40 ambayo ilikuwa inaenda katika miradi ya maendeleo, iende kama ilivyopangwa ili kuimarisha na kuhakikisha kwamba miradi ya maendeleo ya wananchi wetu inazinduliwa na fedha ya Serikali inatumika vizuri.

MHE. ESTHER N. MATIKO: Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chege kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nilikuwa nataka nimpe taarifa tu Mheshimiwa Jafari kwa anachokisema cha kuweka shilingi bilioni 1.7 then ikashuka kuja shilingi bilioni 1.5. Huo umekuwa ni ugonjwa ambapo wanajiwekea malengo madogo hafu baadaye wanakuja wanasema tumekusanya zaidi ya asilimia mia moja na kitu, kwamba tumefikia malengo zaidi ya asilimia na kitu. Kwa hiyo, ni ugonjwa ambao uko nchi nzima. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Chege, taarifa hiyo unaipokea?

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea taarifa hiyo. Hili ndiyo kusudio; na ukisoma taarifa ya CAG ameizungumza hii hadharani kwamba Halmashauri nyingi zinajiwekea mapato madogo ili mwishoni wakikusanya asilimia 50 wafurahi na kujipongeza. Tunajiuliza, tunamfurahisha nani? Kwa sababu kwa kufanya yale, siyo tu kwamba tunataka kumfurahisha mtu, tunapunguza fedha ambazo zingekwenda kwenye miradi ya maendeleo inayowagusa wananchi. Sasa angalia mnatuambia asilimia 10 ndiyo iende shughuli za maendeleo, haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kwanza irudishe, lakini pili, kama siyo Wizara yako imefanya hili, kuna mtu ambaye ali-temper na maelekezo na maazimio ya Baraza la Madiwani, mchukulie hatua. Mheshimiwa Waziri kwenye hili nakuomba sana uwe mkali ili kuweza kurudisha haya tuliyokuwa tunayazungumza.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Chege.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipatia nafasi na mimi kutoa mchango wangu kwenye Wizara ya Ardhi na Maendeleo ya Makazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimekuwa nikisema awali, mimi ni mdau lakini nimekuwa mtumishi zaidi ya miaka kumi kwenye Wizara hii. Kwa hiyo, nikisimama huwa napenda ni-declare interest kwa maana kwamba Wizara hii ndiyo imenilea, maoni yangu na ushauri wangu nitatoa kulingana na taaluma yangu niliyonayo kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze tu kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa namna ambavyo anapambana. Anatusaidia Wabunge lakini lengo lake ni jema kuhakikisha angalau kunakuwa kuna ustawi kwenye sekta ya ardhi kupunguza migogoro, angalau ardhi sasa iwe katika sehemu, itumike kama sehemu ya uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, pamoja na Watendaji wote wa Wizara kwa kazi kubwa wanayoifanya, natambua changamoto zipo nyingi lakini kwa kuwa Wizara ndiyo Wizara Mama na inabeba sekta nyingi lazima mkutane nayo na nichukue nafasi hii kuwapongeza sana namna mnavyopambana kuhakikisha mnayatatua yale ambayo yanapaswa na mnaweza kuyafanyia kazi. Niwapongeze Watumishi ndani ya Wizara hii kwa namna ambavyo na wao wanaendelea kuhakikisha angalau nia na dhamira ya Mheshimiwa Rais inatimia kwa wakati wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kusema naunga mkono hoja mapendekezo ya Kamati yale yote yaliyotolewa na ninaamini kabisa yanatoka kwa nia njema Wizara imesikia na Serikali imesikia itakwenda kuyafanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo mambo mawili leo ya kuchangia, kwanza ningetamani sana nichangie kuhusu chanzo cha migogoro nchini. Kwa study yangu ya kawaida tu inaniambia kwamba moja ya sababu ambayo inaweza kuwa inasababisha migogoro kwa sasa kwenye Taifa letu Tanzania ni kupitwa kwa sera ya ardhi na maendeleo ya makazi hilo ni la kwanza kabisa kwa sababu sera tunayoitumia ni ya mwaka 1995 haiendani na kasi ya uzalishaji na shughuli za kiuchumi za wananchi wanazofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, population iliyokuwa wakati sera inatungwa 1995 haiwezi kuwa sawa na population ya sasa na namna ya shughuli za uzalishaji zinavyofanyika. Kwa hiyo, kwa namna moja au nyingine lazima kutakuwa na mwingiliano wa namna moja kwenda sehemu moja na sehemu nyingine. Pili ni kukosekana kwa mpango wa matumizi bora ya ardhi kwenye ngazi za vijiji. Hili na lenyewe linaweza likawa linachangia kwa kiasi kikubwa sana; na jambo la tatu ni muingiliano wa Wizara za Kisekta, muingiliano kati ya Wizara ya Ardhi, Maliasili na TAMISEMI. Haya yote ya muingiliano huu wa shughuli za kiuchumi zinazofanyika yanatokana na kutokuwa na sera iliyopitwa na wakati. Ndiyo maana mimi nimekuwa nikikuomba sana kwamba jitahidi sana kwa namna moja inayowezekana sera ya ardhi ndiyo chimbuko na solution kubwa inayoweza kutatua changamoto hizi ambazo zinajitokeza kati ya muingiliano wa Wizara na Wizara lakini pia na maeneo ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo jambo hapa kuhusiana na migogoro. Utakubaliana na mimi, migogoro mingi ya ardhi kwenye maeneo mengi kwanza inatugombanisha Wabunge na wananchi lakini mbili inaigombanisha Serikali na wananchi, tatu inagombanisha Chama na wananchi, pia inagombanisha kati ya jamii moja ya wananchi sehemu moja na sehemu nyingine. Sasa kwa namna tunavyokwenda na kutatua migogoro tumeona migogoro mingine pia inatugombanisha kati ya Wabunge na Wakuu wa Wilaya na Wakuu wa Mikoa kutokana na maelekezo wanayopewa ya kusimamia na kutatua ile migogoro na wengine hatupendi haya yatokee, kwa hiyo hii Mheshimiwa Waziri lazima uitazame sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mfano kwangu Rorya nina mgogoro, siwezi kuita ni mgogoro ni sintofahamu ya eneo la Utegi kati ya Kitongoji cha Kiwandani na Begi. Siwezi kuita mgogoro kwa sababu katika vijiji 975 vilivyoainishwa vyenya mgogoro nchini ambavyo Mawaziri wanapita hivi vitongoji havimo, lakini unaweza ukaona sasa hivi tumekwenda tumetengeneza taharuki pale, tunawaambia wale wananchi zaidi ya kaya 300, wananchi zaidi ya 1,200 wahame hawalipwi fidia wanalipwa uwezeshaji peke yake, sasa tunataka kutengeneza mgogoro ambao hauna tija.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nichukue nafasi kukuomba sana Mheshimiwa Waziri kwa kipekee kabisa naamini hili unaliweza, jambo la kwanza twende na maoni ya wananchi wanacho sema. Wananchi wanasema kabla hatujafika huko, kwanza tusimamie Sheria ya kushirikishwa kwenye mikutano waambiwe dhumuni ni nini la wananchi kuondoka eneo lile na hii ndiyo Sheria ya uthamini inavyotaka. Ningeomba sana hili lifanyike. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili wananchi hawa wasingependa uendelee utaratibu wa kuitwa wao ni wavamizi, wana miaka zaidi ya 60 pale, wana miaka zaidi ya 70. Shule ya Msingi pale imejengwa toka mwaka 1959, tukiwaita wavamizi kwamba waondoke bila kuwalipa tunakwenda kutengeneza mgogoro mwingine na lengo la Wizara ni kupunguza na kuzuia mgogoro, mimi kama Mbunge nisingependa kwenye kipindi changu hiki nizalishe mgogoro kwenye Wilaya yangu ya Rorya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo manufaa mengi ambayo tumeyapata kupitia kazi kubwa anayoifanya Mheshimiwa Rais, tumepata maji, tumepata miundombinu ya barabara, nisingetamani tena tuende tukatengeneze mgogoro mwingine ambao utanikwamisha mimi kama Mbunge kutimiza wajibu wangu. Mheshimiwa Waziri ndiyo maana naomba sana haya matatu ambayo wananchi wanaomba, moja kushirikishwa kwenye vikao, mbili kutokuitwa hili jina, lakini tatu ikibainika wanatakiwa kuhama walipwe fidia stahiki kwa mujibu wa Sheria. Wale wananchi hawajagoma lakini wanachogoma ni ushirikishwaji na wanavyoona namna wanavyotaka kupelekwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri utakubaliana na mimi kabla tunakwenda kutamka juzi hakuna kiongozi aliyewahi kwenda kukaa nao wale wananchi akawaambia ABC, kwa hiyo ukija ukitamka vile maana yake unakwenda kutengeneza mgogoro mwingine ambao hauna tija na hauna afya kabisa kwenye Wilaya yangu ya Rorya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, lipo jambo linazungumzwa hapa na mimi niombe sana Mheshimiwa Waziri chukulia hii changamoto siwezi kuita changamoto, chukulia haya maoni ya Waheshimiwa Wabunge yanayotoka ndani ya Bunge kama ni sehemu ya kukutakia mema na wanakupenda sana na mimi nitajenga hoja kwenye hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi, Ukurasa wa 120, Ibara ya 74 inasema, kwa miaka mitano kwa maana ya 2020 mpaka 2025, vijiji vinavyotakiwa kupangiwa matumizi bora ya ardhi ni 4,131 Ilani inatamka. Mpango wa Tatu wa maendeleo unasema angalau kufika 2025/2026 tuwe tumepanga matumizi bora ya ardhi. Naomba hapo nieleweke, kupanga matumizi bora ya ardhi sizungumzii kupima. Kupanga matumizi bora ya ardhi angalau kufikia asilimia 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais hapa ndani alipokuwa anahutubia Bunge alikazia hili kwamba angalau kufika 2025 tuwe tumepanga matumizi bora ya ardhi ya asilimia 50 ya vijiji vyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vijiji tulivyonavyo sasa ni 12,318, tulivyopanga toka uhuru ni elfu mbili mia nane kumi na kitu, maana yake ni asilimia 23 peke yake, lakini kwa miaka mitatu ilikuendana na Ilani, ilikuendana na mpango, ili kuendana na maelekezo ya Mheshimiwa Rais kwa miaka mitatu tumepanga vijiji 681 peke yake. Wabunge wanachosema Mheshimiwa Waziri, kwa kuwa haya yote tunatambua ambao tumekuwa kwenye Wizara hii muda mrefu tunajua yote haya yamekuwa ni changamoto kwa sababu ya ukosefu wa fedha, tunashindwa kutimiza haya matatu ambayo ni maelekezo kwa sababu ya ukosefu wa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri sasa umepata fedha, tumepewa mkopo zaidi ya bilioni 345 tunachotakiwa pale ni kutenga bilioni 60 peke yake unakwenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa kupanga vijiji vyote 4,131, unakwenda kutekeleza mpango wa tatu wa uchaguzi, unakwenda kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais lakini utakwenda kutengeneza legacy kubwa sana kwenye nchi hii kwa sababu kutoka uhuru wewe ndiyo utakuwa umepanga matumizi ya vijiji vingi kuliko wakati mwingine wowote, utakuwa umetengeneza legacy kubwa sana kwa Mheshimiwa Rais. Kwa sababu kama toka uhuru tunazungumza vijiji 2,600 tukipeana miaka mitano sasa tukapanga vijiji elfu nne na kidogo maana yake Mheshimiwa Waziri unakwenda kutengeneza legacy na wataalam ambao tuko kwenye sekta ya ardhi hatutakusahau kwenye hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri ndiyo maana, mimi nikuombe maoni yote ya Waheshimiwa Wabunge yanayotolewa humu yachukue kama sehemu ya kuboresha ili angalau tuende tufike mahali fulani. Tunaamini uwezo wako, tunaamini unaliweza hili, kama utachukua haya yanayozungumzwa ukafanya adjustment ya ule mkopo, uka- impose fedha kwenye Tume ya Mipango, ukaipa maelekezo kuhakikisha wanapanga matumizi bora ya vijiji hivi kupunguza migogoro, utakuwa umefanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuambie Mheshimwa Waziri migogoro hii haina tija kwetu kwanza kama nilivyosema inatugombanisha na wananchi lakini kutokupanga matumizi maana yake umepunguza thamani ya kile Kijiji chenye ardhi, lakini pili inatusumbua sana wanapokuja wawekezaji. Leo akija mwekezaji ambaye anataka kuwekeza Wilaya ya Roya hatuna land bank, hakuna mahali anapofika akaambiwa hili eneo ni kwa ajili ya viwanda ukienda Wilaya ya Rorya, hili ni kwa ajili ya kilimo, hili ni kwa ajili ya ufugaji, hili huwezi kwenda kwa sababu kuna hifadhi, kwa sababu eneo lote limepangwa matumizi halisi, hiyo land bank hakuna kwa hiyo Mheshimiwa Waziri mimi nikuombe sana kwa unyenyekevu mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya yanayozungumzwa kwa sababu yamezungumzwa na Kamati, tumeyashauri mwaka jana tumeyashauri mwaka huu kama kuna uwezekano wa kufanya adjustment ya mkopo huu ili kuleta maslahai ya Taifa, ili kwenda kugusa maeneo mengi, kupunguza migogoro ya Wabunge wanayozungumza humu, ningetamani sana ulione hili na hili linkwenda kukubeba mimi nikutie moyo kwa namna yoyote hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri na kama kuna mtu anakwambia hili litakuharibikia haliwezi, ndiyo maana nikasema unakwenda kutengeneza historia kwa kupunguza migogoro ya wananchi wanaumizana kule nje. Mheshimiwa Waziri mimi naamini sidhani kama unapendezwa leo tuko hapa ndani unasikia kati ya mkulima na mfugaji wanapigana, unasikia kati ya maeneo ya hifadhi wananchi wameingilia. Kuna maeneo ya vishoroba ambayo Tembo wanapita kwenye vishoroba wanaingia kwenye maeneo ya wananchi, wananchi wanakufa maeneo yale, kwa nini hakuna mpango bora wa matumizi ya ardhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisikiliza sekta ya maliasili wanakuambia solution hapa ni kupanga matumizi bora ya ardhi kwenye maeneo haya. Mheshimiwa Waziri nikuombe kwa haya ambayo nimeyasema mimi naamini kabisa kesho utakuja kuyatolea maelezo vizuri na niseme tu kweli kesho nisiporidhika nitakuwa miongoni mwa watu wa kushika shilingi kwenye hili ili angalau niweze kupata ufumbuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote nichukuwe nafasi hii kwanza kukushukuru wewe mwenyewe binafsi na niseme tu niendelee kukutia moyo niseme uendelee kufanya kazi ukiamini Wabunge wengi wako nyumba yako wala usiwe na hofu na yoyote yanayoendelea mtaani au kwenye mitandao ya kijamii, tuko nyuma yako na tunaelewa nini unafanya kwa wakati huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa kuchangia wizara hii nichukuwe nafasi kumshukuru Mheshimiwa Waziri wa Maji Wizara nzima pamoja na wadendaji wa RUWASA, mheshimiwa Waziri pongezi zote tunazokupa tunakupa kwasababu unatimu nzuri kwa maana ya wizara nzima yenyewe namna ilivyofanya kuanzia Katibu Mkuu na watumishi wote, lakini na RUWASA kwa utekelezaji mzuri wanaoufanya hasa pale unapokuwa unapokuwa umetoa maagizo.

Mheshimiwa Spika, nichukuwe nafasi hii kukushukuru binafsi kwa miradi mbalimbali ambayo umenisaidia, mradi wa Shilati niliwahi kusema ulikuwa na Zaidi ya miaka 15 hauna maji, umefanya Ziara ya siku moja ukatamka neno hivi ninavyozungumza tayari wananchi wale wana maji, nikuombe sasa kwa sehemu iliyosalia ulimalizie fedha walioomba milioni 300 ili angalau maji yaweze kusambaa ndani ya kata yote, lakini ikibidi na kata vijiji jirani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini ukuhishia hapo uliweza kunisaidia pia kwenye vijiji vingine kwa mfano kijiji cha Mwame, Kata ya Komuge, umenisaidia Nyarombo, umenisaidia Sudi, umenisaidia Nyehara na vijiji vingine, niendelee kusema kwa namna unavyokwenda sisi vijana tunafarijika sana. Sasa niseme tu usife moyo, ninachoweza kushauri kwa miaka hii inayokwenda ili angalau tuendelee sisi kukuunga mkono na kwenda na wewe sambamba nitakuwa na ushauri kwa maeneo matatu.

Mheshimiwa Spika, moja nikuombe sana Mheshimiwa Waziri jitahidi sana kuboresha RUWASA kwa maana wakala ya maji vijijini, na katika kuboresha huko wajengee uwezo ili waweze kupata watumishi wa kutosha kwa sababu nilikuwa najaribu kuangalia hotuba yako, kwenye fedha za maelendeleo peke yake maji vijijini Tanzania nzima umetenga Zaidi ya bilioni 360, kwa Mkoa wangu wa Mara umeniwekea Zaidi ya bilioni 21, tazama halmashauri peke yangu Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini yako umenipa Zaidi ya bilioni
5.3 ambayo inatakiwa itekelezwe kwa mwaka mmoja wa bajeti.

Mheshimiwa Spika, lakini fedha yote hii kama kuna mtumishi mmoja tu ndani ya halmshauri kwa maana ndiyo engineer utaona namna gani fedha bilioni 35.3 inakwenda kusimamiwa na mtumishi mmoja ambaye inakwenda kusimamiwa na mtumishi mmoja ambaye unaweza kusema ni engineer wa wilaya. Kesho yake naamini, Mheshimiwa Waziri kama usipo wapa uwezo hawa watu wakuongeza watumishi utapita kwenye ziara yawezekana huyu asiwe na wakati mzuri. Niombe sana tuwajengee uwezo watu wa RUWASA ili waweze kuongeza watumishi wa kutosha waweze kukusaidia kusimamia fedha hizi nyingi ambazo mmezitenga kwa ajili kwenye upande wa maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pili nikuombe sana fedha hizi ambazo zimetengwa ziende kwa wakati kwasababu leo nitaondoka naenda kusema na ninasema kwa uwazi kabisa kwamba Mheshimiwa Waziri kupitia Serikali ya Chama cha Mapinduzi chini ya Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan wilaya yangu imepata bilioni 5.3 kwa ajili ya miradi ya maji, ikienda kwa wakati na ikafika sahihi hautakuwa na ugomvi wowote na Mamlaka za usimamizi wa Maji kote hata hao watu wa RUWASA, kwasababu zitakuwa zinakwenda kwa wakati na wanatimiza yale ambayo wananchi wanahitaji haya mawili, Mheshimiwa Waziri ukiyasimamia vizuri ni Imani yangu, pongezi zote wanazozitoa ndani ya Bunge hili utaendelea kupata kwa miaka yote, kwasababu utawajengea uwezo miradi itakwenda kwa usahihi na kwa muda ambao umepangwa, niamini sana niendelee kukuomba sana fedha hizi ambazo zimetenga, hasa Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, niombe sana Wizara ya Fedha kwa kushirikiana na Wizara ya Maji fedha hizi mtusaidie sana ambazo zimetengwa kwenye bajeti hii tutengeneze historia kwa mara ya kwanza kwa fedha zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya maji kwenda yote kwa asilimia 100 hasa kwenye miradi ya maji hasa mkizingatia Rais Mheshimiwa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan ni mama ambaye kimsingi na yeye angetamani wamama wote ndani na vijiji vyote ambao kimsingi wanateseka sana na kero ya maji kwa miaka hii michache waweze kuondokana na kero hii ningeshukuru sana kama haya na hii bajeti tuliyoitenga itakwenda kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, nizungumzie sana hii miji 28. Mheshimiwa Waziri nikupongeza sana mwanzoni ilikuwa inazungumzwa 16 lakini leo ndani ya Bunge hili unazungumzia miji 28. Nikuombe usipunguze hata mji mmoja, nenda nayo miji 28 kama ilivyosema kwa sababu tayari ndani ya Bunge hili tunaondoka tukijua miji 28 inakwenda kupata maji ya uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ndani ya jimbo langu nina vijiji 87 lakini vijiji vyenye maji ni 12 peke yake. Vijiji ambavyo vina miradi ni 23; vijiji 52 ndani ya jimbo langu havina mradi wowote wa maji safi na salama. Kwa hiyo, mradi huu wa miji 28 leo hii ukipitisha bomba lile linalotoka Rorya kwenda Tarime maana yake zaidi ya kata 11 zinakwenda kunufanika na mradi huu. Ndiyo mradi ambao sisi watu wa Rorya tunategemea kwa muda mfupi utakuwa umetatua kero kubwa na kwa eneo kubwa. Coverage ya mradi huu ni kubwa sana kuliko hata ukichimba kisima kimoja kimoja kwenye kila Kijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwenye huu mradi wa miji hii, naomba Waziri uipe kipaumbele sana hasa Rorya na Tarime. Watu wa Tarime hawana ziwa, ili wapate maji wanategemea maji ya Ziwa Victoria ambayo kimsingi yanatokea Rorya, Kijiji cha Nyamagaro. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ukisimamia hili ni imani yangu kwa muda mfupi ndani ya miji hii miradi ya maji itakuwa mizuri na utakuwa umetatua kero kwa asilimia kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho, Waziri amesema kuna watu wanapita kukagua miradi iliyotekelezewa na Serikali kwa miaka mitano iliyopita kwa kutumia wakandarasi na inawezekana wasiwe wakandarasi lakini fedha zilizokwenda kwa ajili ya miradi ya maji haikutumika sawasawa. Naomba Waziri atilie mkazo suala hili kwa sababu kama fedha zinaendelea kwenda kulekule ambako hakujatengenezwa mfumo mzuri wa kusimamia miradi hii na kuna fedha ilikwenda haikutumika inavyotakiwa maana yake hata hii inayopelekwa yawezekana isitumike vizuri. Naomba sana ukamilishe suala hili ili kila kitu kiende sawasawa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Nishati
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Wizara hii ya Nishati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwanza kwa kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutoa fedha nyingi kuiwezesha Wizara hii lakini pia kuhakikisha angalau miradi mingi ya kimkakati na miradi ambayo kimsingi ndiyo msingi wa uchumi na uzalishaji wa umeme inakwenda kutimia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili nami naungana na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa dhati kabisa kwa namna ambavyo anaendelea kuwashika mkono na kuhakikisha angalau Wizara hii inaweza kutimiza yale ambayo ni malengo halisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo kwanza ulivyo mbunifu, ulivyo mpole, namna ambavyo unasikiliza hoja za Wabunge, pia naamini kabisa namna ambavyo umeamua kutengeneza mfumo upya na kuliunda Shirika (TANESCO) kwa maslahi mapana ya Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kukuomba sana kama kijana mwenzetu uendelee kuwa hivyo, ninaamini kabisa kwamba ukiendelea kuwa hivyo basi utatufikisha mbali sana kwenye hili ambalo ni kusudio letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kwanza pia kukushukuru sana, pamoja na kwamba mwanzoni tulianza kusuasua katika utekelelezaji wa umeme wa REA kwenye Wilaya yangu na Mkandarasi anayeitwa GIZA Cable, nitumie nafasi hii kukushukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa namna ulivyoingilia. Leo mimi nazungumza, katika vijiji 13 vilivyokuwa vimesalia kwa ajili ya kupeleka umeme wa REA, vijiji vyote sasa ninavyozungumza tayari umeme umefika na amebakiza vijiji viwili tu kuweza kuwasha umeme huo. Kwa hiyo, ni jambo la heri na mimi niendelee kuwashukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza na wewe Vijiji vya Nyihara, Kenyamsama, Borere, Wamaya, Urio, Tabati, Nyamusi, Nyahera pamoja na Masike, tayari umeme umeshafika, vimebaki vijiji viwili tu kwa ajili ya kuwasha. Nitumie nafasi hii kuwashukuru sana watendaji wa TANESCO kwa kusimamia hili na kuhakikisha angalau linatekelezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na haya ambayo tunakupongeza na kukushukuru, nadhani leo tukushauri, ninatamani nikushauri maeneo mawili ili angalau uendelee kufanya mazuri zaidi kwa maslahi mapana ya Taifa. Kwanza, nimesikiliza hotuba yako na nikiangalia kwenye aya ya 22 ya hotuba yako ambapo ulikuwa unazungumzia hali ya uzalishaji wa nishati umeme na mahitaji halisi ya wananchi juu ya uzalishaji kutumia nishati ya umeme, mwenyewe kabisa kwenye hotuba yako kwenye aya ya 22 umekiri hadharani kwamba haiendani na kasi na namna ambavyo wananchi wanahitaji umeme na uzalishaji wenyewe ulivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia ukienda kwenye vipaumbele vyako kwenye hiki kitabu ulichotupatia, kipaumbele cha kwanza kabisa umezungumzia hilohilo, kwamba ni kuhakikisha angalau vile vitongoji vyote vilivyosalia, vitongoji 36,101 vinapata umeme safi na salama. Pia ukienda kwenye aya ya 113, mpango maalum wa kuhakikisha kwamba angalau umeme wa REA unafika kwenye maeneo ya vitongoji vyote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukisikiliza haya yote maana yake kuna jambo ambalo nadhani unakusudia kulifanya lakini kwenye hotuba yako humu ndani labda hujaliweka sawa. Ninatamani sana utakapopata nafasi ya kufanya majumuisho kesho utuambie mpango mkakati uliojipanga kuhakikisha angalau vitongoji vyote 36,101 vinafikiwa na umeme nchi nzima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utakumbuka na utakubaliana na mimi kwamba kila wakati ukisimama ndani ya Bunge unaona Wabunge namna wanavyohoji umeme ndani ya vitongoji. Nami mwenyewe ndani ya Jimbo langu nina vitongoji 507, lakini vitongoji ambavyo vina umeme havizidi 200. Kwa hiyo, maana yake zaidi ya asilimia 60 ya vitongoji vilivyosalia havina nguzo wala miundombinu yoyote ya umeme, na ndivyo ilivyo katika maeneo yote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu dhamira yako umeionesha kwenye hotuba yako, ningetamani mwishoni Mheshimiwa Waziri utuambie, na usiogope, kama kuna namna nyingine bora ya kupata fedha, tuambie Bunge hili lijue, kama kuna namna ya ku-impose hata rate kidogo kwenye gharama za mafuta kwa maana ya shilingi 50 mpaka shilingi 100 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba umeme unapata fedha nyingi, zaidi ya shilingi trilioni 6.7, kwenda kutatua vitongoji vyote nchi hii, wewe tuende huko useme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu Mheshimiwa Rais amekuwa akilizungumza hili, kwamba ndani ya miaka mitano matarajio yetu ni kwamba vitongoji vyote 36,000 vinakwenda kupata umeme. Sasa Mheshimiwa Waziri ukiliacha hili likawa fumbo na kuendelea kututesa maana yake inawezekana ndani ya miaka mitano usilifikie. Nenda fanya kazi, fanya utafiti, kaa na Wizara ya Fedha, hata ikibidi kama unaweza kuweka shilingi 50 mpaka shilingi 100 kwenye nishati ya mafuta ili angalau iweze kuzunguka nchi nzima ili vitongoji vyote viweze kupata umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ambacho ninatamani nikushauri pia ni namna ya utekelezaji wa umeme kwenye maeneo ya Miji ambayo inakua. Mimi nina Mji pale unakua unaitwa Shirati, tumekuwa tukiuita Mamlaka ya Mji Mdogo lakini ni mamlaka ambayo haina GN, haipo kisheria, hata uki-google hapo Mamlaka ya Mji Mdogo Shirati hautaiona, lakini rates wanazochajiwa wale wananchi, wanalipa zaidi ya shilingi 321,000 kwa nguzo moja wakiambiwa kwamba ile ni Mamlaka ya Mji Mdogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hawajapata usajili hakuna GN, hakuna mratibu na wala haijiendeshi iko chini ya Halmashauri, ninaomba sana Mamlaka ya Mji Mdogo, kwa maana ya Shirati, Kata za Mkoma na Raranya, tuendelee kuwaungia umeme kwa bei ileile ya zamani, shilingi 27,000, badala ya kuwaongezea bei. Kwa sababu tunawaongezea bei kwa sababu ile ni Mamlaka ya Mji Mdogo lakini mamlaka haipo, kwa hiyo inatengeneza taharuku na sababu ambazo hazipo. Ningetamani sana kesho wakati wa majumuisho utamke tu kwamba wananchi wa maeneo haya, hizi Kata mbili, kwa sababu bado mamlaka haijaanza kufanya kazi, haipo na haijasajiliwa, basi waendelee kuunganishiwa umeme kwa bei ileile wenzao wa vijiji vingine wanayounganishiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine katika hilo ni fidia ya wahanga wangu ambao walikubali toka 2011. Nilikwambia hili kwamba waliridhia kwa hiari yao kupisha umeme mkubwa uwe maeneo mengi, vijiji vingi tu. Zaidi ya wananchi 200 toka mwaka 2011 hawajalipwa fidia. Ninaomba pia kesho ukipata nafasi utamke juu ya hawa wananchi. Kwa nini toka 2021 Mkoa mzima wa Mara vijiji vyote vimelipwa kasoro Wilaya yangu ya Rorya. Wilaya zote zimelipwa kwa ajili ya kupisha umeme ule kasoro Wilaya yangu ya Rorya. Hawa wananchi wamekuwa wakifuatilia kwa muda mrefu, kwa hiyo niombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu nilikuambia mwaka jana ninaamini kesho ukipata ridhaa ya ku-conclude utatoa tamko juu ya adha hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu katika hilo ni hawa watu wa ETDCO hii kampuni tanzu ambao wanafanya kazi. Yawezekana ikawa inafanya kazi vizuri sana, nimeona humu wanazungumza wanapata faida mpaka bilioni mbili na pointi kwa mwaka, lakini kwangu nadhani kuna sehemu hawajafanya vyema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, toka mwaka 2021 leo ni 2023, wamepewa miradi mitano, hawajawahi kufika hata mradi mmoja. Sasa haya ndiyo yanaleta manung’uniko mengi, wakati mwingine Mheshimiwa Waziri unaweza ukavishwa mzigo ambao siyo wa kwako. Kama ETDCo hawana uwezo bado wa kufikisha umeme maeneo haya, apewe Mkandarasi mwingine ili apeleke vitongoji hivi vyote alivyopewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ana miradi maeneo matano, na nitakutajia, anayo Kasino, Kongo, Isegere, Buturi, Kyamwama na Nyamunga. Maeneo haya toka 2021, leo tunazungumza 2023/2024 hakuna Mkandarasi site wala chochote kinachoendelea. Kwa hiyo, unaweza ukaona wananchi wana haki ya kulalamika lakini kuna mtu mwingine tu ambaye amepewa mradi inawezekana anashindwa kutimiza. Niombe na lenyewe hili utakapopata nafasi kesho uweze kulisemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni kukatikakatika kwa umeme. Mimi Wilayani kwangu, kama nilivyokuwambia sehemu kubwa ya uzalishaji inategemea umeme. Kwa sababu umesema kwamba sasa hivi unaweka fedha kwa ajili ya kuboresha miundombinu, niombe sana Wilaya ya Rorya uingalie, kwa sababu mpaka sasa ninapozungumza na wewe haiwezi kupita wiki, siku tatu umeme haujakatika, unakatika kwa sababu ya miundombinu inawezekana ikawa imechoka sana. Kwa hiyo, nikuombe kwenye hili nalo uone namna unavyoweza kunisaidia kwenye upande huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyotangulia kusema, unafanya kazi vizuri sana, maeneo haya yote unayofanya kazi unafanya kazi kwa ushirikiano na Wabunge, kwa sababu bado ni mtu ambaye unasikiliza maoni na ushauri wa Wabunge, niendelee kukuomba endelea hivyohivyo kwa sababu msingi na dhaminra yako ni njema huko mbele utakapokwenda. Kwa hiyo, ninaomba haya niliyoyasema kwa nia njema kabisa kwa maslahi ya watu wangu wa Rorya ili uweze kuwakumbuka, ninatamani sana kesho, kama nilivyosema utoe angalau majibu kwa sababu haya yamekuwa yakilalamikiwa miaka nenda rudi. Suala la Shirati, kama nilivyosema, walipe 27,000 kama wanavyolipa maeneo mengine, kwa sababu bado hakuna mamlaka, hii ndiyo imekwamisha sasa shughuli za kiuchumi na kuvuta umeme pale limekuwa dogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi. Kwanza nianze kukushukuru mwenyewe binafsi kwa kuridhia na kunipa nafasi na mimi niweze kutoa maoni yangu kwenye bajeti hii ya Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama ilivyo ada, nianze kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kuwa nzuri anayoifanya, hasa mwenyewe kwenye jimbo lango. Hivi nimeongea na Mwenyekiti wiki hii ninaambiwa tumepokea zaidi ya milioni 570 kwa ajili ya ujenzi wa sekondari mpya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya hivyo, nilikuwa na milioni 470 kwa mwaka uliopita pia kwa ajili ya sekondari mpya ya kata isiyokuwa na sekondari. Naendelea kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo anatushika mkono sisi wananchi wa Rorya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu tumekuwa na changamoto ya maji, lakini ninavyosema sasa hivi, katika miradi ya miji 28 tumepewa zaidi ya shilingi bilioni 132 kwa ajili ya utekelezaji wa maji na sasa tunajenga tanki la lita milioni sita kwa ajili ya kuhakikisha tunasambaza maji kwenye Wilaya yetu ya Rorya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana pia kwa kutupa fedha kwa ajili ya ujenzi wa VETA. Kubwa kuliko yote, nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kuridhia kuingiza barabara yetu ya Mika–Utegi–Shirati–Kirongwe, kwa ujenzi wa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii kukuomba sana Mheshimiwa Waziri wa Fedha ulione hili kama fursa, kwa kuwa mama tayari sisi ametukumbuka na ameliweka kwenye bajeti, sasa iende ikatengewe fedha, itangazwe kwa ajili ya ujenzi wa kilometa 56 ili angalau barabara hii kwanza inakwenda kufungua uchumi wa Wilaya ya Rorya pamoja na nchi jirani, lakini pia inakwenda kufungua uchumi wa Mkoa mzima wa Mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninyi kama Serikali, kwa sababu barabara inakwenda kutuunganisha kati ya nchi na nchi, naamini kabisa mnakwenda kuvuna na kupata mapato kwa asilimia kubwa sana kupitia barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii pia kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa namna kwanza ulivyojipambanua kwa namna ulivyokuwa unawasilisha hoja. Lakini pili, kwa namna unavyoendelea kumshauri Mheshimiwa Rais kusimamia sera zinazohusiana na sekta na Wizara hii ya Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa mambo matatu; la kwanza, nikushukuru sana kwa namna ambavyo umeweza kumshauri Mheshimiwa Rais kuridhia na kufuta ada kwa wanafunzi ambao wanasoma vyuo vya ufundi. Kwa kweli Mheshimiwa Waziri hili umewasaidia sana wananchi wanyonge, hasa sisi Wabunge wa vijijini hili lilikuwa ni kimbilio kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili; ni kuridhia kwenye vyuo vya kati kuendelea kutoa mikopo kwa wanafunzi angalau waliochaguliwa kwenda maeneo hayo. Kwenye hili Mheshimiwa Waziri ningeomba nikushauri na ulitazame na ninaamini mwishoni uweze kuliwekea majumuisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati unatoa hotuba yako hapa ulijipambanua hadharani, wazi kabisa, na wananchi wote walikujua kwamba wewe ni mtoto wa mkulima, ni mtoto wa mfugaji, na umelelewa katika mazingira magumu sana. Wapo wananchi huko chini Mheshimiwa Waziri, kwa huu huu mkopo ambao tunakwenda kuutoa, maana yake ni kwamba tukisema tunatoa kwa badhi ya wanafunzi waliochaguliwa kwa baadhi ya kozi na kozi nyingine tusiwape mkopo, tunakwenda kutengeneza mpasuko sana huku chini kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, litazame Mheshimiwa Waziri; leo mtu na jirani yake, anamtazama mtoto wa kwake anakwenda kusoma chuo fulani anapewa mikopo lakini huyu ambaye amechaguliwa na Serikali kwenda chuo fulani hapewi mkopo, lakini wote wanaishi maeneo yaleyale, wote ni wajane, wote hawana fedha na wote ni maskini kabisa wa kutupwa. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri ulione hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu nimechangia hapa, na ninaamini wananchi wanakuona, na wewe umejipambanua kama role model wa aina ya jamii fulani wanaotoka huko, litazame hili, ikiwezekana wanafunzi wote wanaokwenda kwenye vyuo vya kati wapewe mikopo, haijalishi huyu anakwenda kusomea nini na anasomea nini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, ukirudi nyuma, hata huyu ambaye hakupenda asome yale masomo kwa mfano ya sayansi, ukirudi nyuma kwenye historia unaweza ukakuta si sababu yake, hakuwa yeye ndiyo chanzo cha kutokusomea sayansi. Unajua shule zetu zina changamoto nyingi sana za walimu wa sayansi kwenye baadhi ya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiwatoa wale ukasema hawa kwa sababu wamechaguliwa kwenda kozi fulani kwa hiyo hawastahili kupata mkopo wanakwenda kupata wanafunzi fulani, utatutengenezea deni kubwa sana sisi Wabunge ambalo tulikuwa tumelitua, kwa msaada huu tulikuwa tumelitua. Nilikuwa na wanafunzi zaidi ya 50 ambao walikuwa wanatarajia angalau kufika mwezi Septemba tuwachangie kwa ajili ya kwenda kulipia ada, na ada ya vyuo unaifahamu, ni zaidi ya milioni moja mpaka 1,400,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, sasa litazame; kama mzazi alikuwa anashindwa kulipa 70,000, mama yetu kwa huruma yake akaamua kuiondoa hiyo 70,000 ya ada, leo 1,400,000 huyu mzazi anakwenda kuitoa wapi? Kwa hiyo, ninaomba sana Mheshimiwa Waziri utakapofanya majumuisho, ulikuwa una nia njema, lakini tukiliweka katika mazingira haya tunakwenda kuwagawa Watanzania na haitakuwa imependeza zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru pia kwa namna ambavyo umeendelea kumshauri Mheshimiwa Rais kwa kuridhia kuondoa VAT kwenye nyumba zinazojengwa za kibiashara zenye gharama chini ya milioni 50. Wito wangu ni nini kwenye hili; real estate developers, hasa National Housing, TBA na Mifuko ya Hifadhi ya Jamii inayofanya kazi ya development ya ujenzi wa nyumba, waitumie hii kama fursa ya ujenzi wa nyumba hizi za gharama nafuu ili waendane na malengo na dhamira yako iliyokusababisha kumshauri Mheshimiwa Rais. Ili angalau nyumba za bei nafuu zisizozidi milioni 50 zijengwe maeneo yote ya nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, natamani niwaone Rorya wakija wanajenga nyumba milioni 25 kwa ajili ya kuwasaidia watumishi. Waende halmashauri nyingine wajenge nyumba milioni 30, nyumba milioni 35. Kwa sababu hawa real estate developers walikuwa wanalia kuhusiana na bei ya nyumba, na wananchi wengi walishindwa kulipia hizi nyumba kwa sababu ya ongezeko la VAT, na Mheshimiwa Rais ameridhia kuiondoa. Ninatamani sana hizi taasisi ziweze kujikita kutumia fursa hii kwa uzuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, lingine ni Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi. Kwa mujibu wa sheria hii ambayo tunayo hapa; The Land Use Planning Act No. 6 ya mwaka 2007 inaipa mamlaka Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, hawa ndio wanapewa mamlaka makubwa ya kupanga na kuainisha matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo kwenye mpango wako wa Tatu wa Taifa wa mwaka 2022/2023-2025/2026, anayekwenda kutafsiri ile asilimia 50 ya kuainisha mpango wa matumizi bora ya ardhi ni hii Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi; anayekwenda kutafsiri Ilani ya Chama cha Mapinduzi, ukurasa wa 120, kwamba ni lazima tutakapofika 2025 vijiji viwe vimepangwa matumizi zaidi ya 4,131 ni Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, anayekwenda kutafsiri hotuba za viongozi zinazozungumzia mpango wa matumizi bora ya ardhi ni hii tume. Na ndiyo maana kwenye sheria hii hawa ni National Planning Authority ambao kimsingi wanatakiwa wasimamie haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wewe Mheshimiwa Waziri utakuwa shahidi, hawa watu wamefanya kazi kubwa sana Msomera, wamefanya kazi Loliondo, sasa hivi wako Bunda, wanafanya kazi Tarime. Na hawa ndiyo wanahakikisha wanapanga matumizi bora ya ardhi kwa wale wananchi waliohamishwa Ngorongoro kwenda kule Msomera; wamefanya kazi kubwa sana nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, ninachosikitika kwa mara nyingi, na nimekuwa nikilisema sana hili; ni kwa nini tume hii, moja, hatuipi meno, lakini mbili, hatuitengei fedha nyingi ili iweze kuendana na Ilani ya Chama cha Mapinduzi, maelekezo ya Mheshimiwa Rais, lakini iendane na Mpango wako wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa. Kwa sababu inaonekana kama ni kitu ambacho hakipo na hakina umuhimu wake. Lakini ninyi ni mashahidi Mheshimiwa Waziri; kama tunataka tuondokane na migogoro nchini ni lazima tume iongezewe fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana wengi tumekuwa tukishauri hapa, kama tatizo ni fedha na nikushukuru sana Mheshimiwa Waziri, mwaka jana tulichangia ukaridhia kuongeza fedha ukawapa bajeti zaidi ya bilioni 5.4. Mwaka huu naambiwa mmeishusha, mnawapa bilini 3.7, na wakati malengo ni yaleyale, na hatujafikia dhamira ya Ilani, hatujafikia dhamira ya Mpango wa Tatu wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo, nikuombe, kwa sababu tuna fedha ya mkopo, ile bilioni 345 mmege zaidi ya bilioni 20, bilioni 30, muwape hawa watu ili waende wakapange watumizi bora ya ardhi nchi. Na ninaamini kabisa kwa kufanya hivyo watakuwa wanatimiza na wanaendana na malengo ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana, naunga mkono hoja. Ahsante kwa kunipa nafasi.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, kwanza nikushukuru nichukue nafasi hii kukushukuru kabisa kwa kunipa nafasi kuchangia Wizara hii nyeti. Lakini pia nachukua nafasi hii kumshukuru Waziri, Naibu Waziri Pamoja na watendaji wote wa Wizara wakitambua kwamba wanaongoza Wizara ambayo ni mtambuka ni Wizara ambayo katika sekta ni Wizara toka tunapata uhuru tunazungumzia Wizara ya Kilimo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni Wizara ambayo ukitaja sekta zingine zote unaweza ukasema zimeanza baada ya Wizara hii ya Kilimo. Lakini nichukue nafasi hii kuwapongeza kwa kazi kubwa mnayoifanya changamoto ni nyingi wakati mwingine kuzimaliza kwa muda mfupi yawezekana isiwe kazi ya rahisi lakini tuna imani kwa sababu sasa tumempata Waziri kijana ambaye ni Professor, tumempaka Naibu Waziri kijana ni imani yangu sasa mtakwenda kubadilisha kilimo kutoka kwenye nadharia sasa iende kwenye vitendo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu kwamba kwa miaka yote toka uhuru hakuna ambacho hakijawahi kuandikwa kwa maana ya research kama utafiti kwenye zao lolote la kilimo nchi hii. Kazi kwenu sasa kwenda kutumia research zilizoandikwa na wataalamu hao ili sasa kutumia nafasi zenu za vijana muiondoe nadhania hii ya kilimo ambayo imekuwa ikizungumzwa na wananchi na Pamoja na Waheshimiwa Wabunge iende kuwa vitendo.

Mheshimiwa Spika, lakini Wizara hii haiwezi kufanya mazuri kama haina fedha angalia tazama bajeti tunayoijadili sasa ni bilioni 2.9 kama haitaenda yote maana yake haya tunayozungumza ukiacha nje ya mifumo hii ambayo Wabunge wamekuwa wakilalamikia, maana yake bado haiwezi kufanya vizuri vile ambavyo wananchi wanahitaji. Nichukue nafasi hii kuiomba sana Serikali hii bilioni 2.9 iliyoombwa na Wizara hii wapeni yote ili angalau tunaporudi bajeti ya mwakani tuweze sasa kushikana mashati sawasawa tukiwa tumewapa fedha sasa za utekelezaji na uendelezaji wa utekelezaji wa Wizaa hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nizungumzie maeneo yangu mawili ndani ya jimbo langu eneo la kwanza ni eneo la kilimo cha umwagiliaji mradi wa Chereche nilikuwa naangalia taarifa ya Mheshimiwa Waziri hotuba yake na randama sijaona ikitajwa. Chereche ni mradi ambao wa umwagiliaji una heka Zaidi ya 350 unahudumia zaidi ya wananchi ambao walikuwa wakifanya shughuli pale Zaidi ya watu 300 na kitu.

Mheshimiwa Spika, mradi huu wa umwagiliaji umeanza toka mwaka 2002, lakini toka mwaka 2018 umesimama una miaka minne tunakwenda miaka mitano umesimama na haufanyikazi yoyote unaweza ukaona wananchi waliokuwa wanafanya shughuli za kiuchumi pale mpaka leo wanaenda wapi. Lakini nimeangalia kwenye bajeti humu nilikuwa naangalia kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri haupo tuna mradi wa umwagiliaji upo Kijiji cha Rabol Kata ya Rabol, Tarafa ya Loimbo una zaidi ya heka 250 kwa mara ya kwanza Serikali iliamua kufufua mwaka 2012 kwenda mwaka 2013 wakaitengea bajeti 2016 kwamba sasa tunakwenda kuufufua huu mradi ili uwanufaishe wananchi wa maeneo yale Kijiji cha Loimbo. Hivi ninavyozungumza mpaka leo ile bajeti 2016 haikwenda kwenye utekelezaji nimeangalia kwenye bajeti ya Serikali bajeti ya Mheshimiwa Waziri haimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini pia tuna mradi wa umwagiliaji Ochuna wananchi wanalima mpunga kule ni mradi wa umwagiliaji ambao wananchi masikini ya Mungu wanahangaika lakini wanachangamoto zao za miundombinu ndani ya ule mradi haipo ni imani yangu Mheshimiwa Waziri atakapokuwa amesimama kesho kufanya majumuisho aniambie na kwa sababu nimekwisha zungumza naye kabla ya hapa haina haja ya sisi tena kurudi kule na wakati ninaye Waziri ndani ya Bunge hili. Atoe tamko na atoe maelekezo wale watendaji wote ambao wamesahau kuingiza kwenye bajeti ili angalau sasa nitakaporudi na mimi Jimboni nirudi nikijua hawa wananchi wanatokaje hapa na wanakwendaje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa kwanza kwa jioni ya leo. Nianze tu kwa kusema naunga mkono hoja ya Bajeti ya Serikali, lakini pia nampongeza Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wasaidizi wake wote Makamu wa Rais, Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri wa Wizara hii kwa bajeti nzuri ambayo kimsingi imekidhi mahitaji na matakwa ya wananchi, lakini pia wame-consider kwa kiasi kikubwa sana maoni ya Waheshimiwa Wabunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza mchango wangu nimwombe tu Mheshimiwa Waziri atakapopata nafasi aweze kuielezea ile factor ya kusema kwamba mtumishi hasa watumishi wa kuteuliwa atakapokuwa amepoteza nafasi yake basi anarudi nyuma kukidhi kwa maana ya kuchukua mshahara ule ambao alikuwa analipwa mwanzo. Yaani maana yake ni kwamba kama mtu alikuwa ni Afisa Mtendaji wa Kata mamlaka zikamwona kutokana na utendaji wake mzuri, akateuliwa akawa Mkuu wa Wilaya, baada ya mwaka mmoja au miaka miwili akapanda akawa Mkuu wa Mkoa, kwa sababu utendaji wa kazi ndiyo unamfanya apande hizo nafasi na namna mamlaka zinavyomwona, lakini pale utumishi wake unaposita anarudi kuchukua mshahara ule wa Mtendaji wa Kata.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbuke kuna miaka mitatu hapa amepoteza, nataka nijue anarudi kwenye mshahara upi? Kwenye mshahara ule wa awali kipindi anateuliwa kwenda kuwa Mkuu wa Wilaya au atarudi kwenye mshahara upi? Kwa sababu hapo miaka mitatu naamini wenzake pia kuna mishahara imeongezeka. Sasa nataka nijue tu na Mheshimiwa Waziri atakapopata nafasi aielezee kwa sababu hii ndiyo watumishi wengi hasa hawa ambao wanakumbwa na nafasi za uteuzi wametengeneza taharuki hiyo. Mtu alikuwa ni Mwalimu analipwa Sh.400,000, ameonwa na mamlaka amekuwa Mkuu wa Wilaya ana-stop Ukuu wake wa Wilaya anarudi kwenye mshahara wa Sh.400,000 ule ule au wata-consider na ile miaka yote ambayo amepoteza kwenye nafasi hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijikite kwenye mchango wangu na nitachangia katika maeneo matatu. Eneo la kwanza, kama nilivyoanza kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, nimesoma vizuri sana bajeti hii na nimekesha vizuri, nimeisoma kwa kiwango kikubwa, lakini niseme na kwa kumkumbusha sekta ya ardhi kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha hajaiweka. Sekta ya Ardhi haijapewa kipaumbele kama zilivyopewa sekta nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisema na tumekuwa tukishauri hapa, ukisoma yale maeneo yote ambayo fedha za Serikali zinakwenda kwenye mahitaji muhimu kwenye sekta mbalimbali, ardhi haijaguswa na nimekuwa nikisema na tumekuwa tukisema hapa Mheshimiwa Waziri atakumbuka ardhi ni rasilimali asilia, ardhi ni mtaji, lakini ardhi pia ni chanzo cha mapato. Bahati nzuri kwenye bajeti hii Mheshimiwa Waziri amesema kwamba dhima ya bajeti ni kwenda kujenga uchumi shindani wa viwanda na maendeleo ya watu. Huwezi kujenga uchumi shindani wa maendeleo ya watu kwenye viwanda kama ardhi haijazungumzwia kwa kiwango hicho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri atakapopata nafasi mwishoni wakati wa majumuisho yake, aje aizungumzie ardhi kama sekta ambayo ni sekta mtambuka, ni sekta ambayo haya mengine yote tunayoyafanya ya uchumi wa maendeleo ya viwanda hayawezi kufanyika bila kuwekeza kwenye ardhi. Ningetamani Mheshimiwa Waziri atakapokuwa anazungumza ajikite kwenye maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais kwa kutambua umuhimu wa sekta ya ardhi, mwaka jana alitoa zaidi ya bilioni 50 kwa ajili ya kwenda kwenye mamlaka za upangaji na upimaji kwa maana halmashauri na ilikwenda kazi ya kupanga, kupima na kurasimisha. Ukisoma kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri haizungumzwi. Pia tunatambua mwaka huu ametenga zaidi ya bilioni 345 ambayo inakwenda kwa ajili ya kuhakikisha hizo kazi za kuboresha miundombinu ya sekta ya ardhi kupanga na kupima na maeneo mengine ningetamani nayo aielezee kwa maana sekta ya ardhi ni sekta mtambuka na kwa kutoa maelekezo namna fedha hizi zitakavyoenda kunufaisha sekta ya ardhi na maeneo mengine. Siyo hivyo tu, tuna zaidi ya bilioni 130 ambazo zimetoka Korea, hii yote ni michango ya Mheshimiwa Rais. Ukisoma kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ardhi ni kama vile haijaguswa kwa ukubwa unaostahili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufanya majumuisho mwishoni aiweke na aizungumze ili angalau mamlaka za upangaji na upimaji na wananchi na wadau wengine wa sekta ya ardhi, lakini wajue ni namna gani ambavyo Serikali imejipanga kwenda kuboresha kwenye sekta ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili ni miradi ya kimkakati pamoja na vyanzo vya mapato ya halmashauri. Kwa kuwa Wizara ya Mheshimiwa Waziri ndiyo imekuwa ikijikita sana kwenye kupanga matumizi na kupeleka fedha za miradi ya kimkakati, zipo halmashauri ambazo ni za kimkakati lakini mapato yake ni madogo sana. Mathalan, Wilaya yangu ya Rorya, ndiyo maana tuliwahi kushauri hapa, ni vema Wizara ya Fedha ikafanya mchanganuo wa halmashauri ambazo zipo mipakani, mapato yake ni madogo, siyo stable, haya-sustain na wakati mwingine wanakusanya kwa kujinyima kweli kweli, hawa ndiyo wapewe fedha za miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unaweza ukaona kwenye mapendekezo ya hotuba ya Mheshimiwa Waziri amesema kwamba sasa tunakwenda kuiboresha, kuichanganua ile 10% iliyokuwa inatoka, kwamba itoke asilimia tano, asilimia mbili mbili. Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi, kuna halmashauri ambazo kwa mwezi wanakusanya milioni 40 peke yake, mfano kwangu Rorya, ukikusanya milioni 40 Rorya, ukitoa asilimia kumi ni milioni nne, ukianza kuigawanya kwa kipindi hiki kwa sasa kwa asilimia 4:4:2, maana yake unaweza ukaona kwamba vijana walikuwa wanapata milioni 1.6 peke yake, Sh.1,600,000 kikundi cha watu 10 wanaitumia vipi!

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa umeenda tena umeinyambulisha, umeigawa, unasema itakwenda 2%, yaani maana yake wale waliokuwa wanapata Sh.1,600,000, kikundi cha vijana 10 wanapata 800,000 kwenye halmashauri zenye mapato madogo kama Rorya. Kwa hiyo naomba kama kuna uwezekano tuiache ile10% iende vile vile 4:4:2, ile fedha 5% ambayo ilikuwa inakwenda kwa ajili ya Wamachinga, tuendelee na mkakati ambao Mheshimiwa Rais ameshatusaidia, amepeleka zaidi ya bilioni 10 kwenye kila mkoa, ziende zikaboreshe maeneo ya Machinga, tusiguse kule, kwa sababu ukigusa kule kwa sababu ukigusa kule, Mheshimiwa Waziri atakubaliana na mimi vijana sasa kwa kasi inayokwenda, kwa growth rate ambayo inakwenda mpaka kufika 2025 kutakuwa na vijana wengi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa tulipo kuna msururu wa vijana, makundi ya vijana wameomba mikopo kwenye halmashauri zetu, lakini hawajapewa. Sasa ukipunguza kile kiwango kwenye halmashauri inayopokea milioni 40, wapo watu 10 wanapokea milioni nane, haitafaa hata kidogo. Kwa hiyo naomba nishauri kwenye hilo, tuone namna ya kulifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, ni namna ya kuboresha kwenye maeneo ya mipaka. Niliwahi kuchangia hapa kutumia fursa za kimpaka kati ya halmashauri ambazo ziko ndani ya nchi na nchi. Kwangu Rorya, Mheshimiwa Waziri atakubaliana nami nimekuwa nikisema hapa tuna Bandari ya Sota, pale ndani ya wilaya yangu, lakini hatujawahi kuona namna gani inanufaisha uchumi wa nchi yetu. Tuna mipaka yetu pale Kirongwe, nichukue nafasi kwanza kuwashukuru watu wa TRA, baada ya kuona nimezungumza kwa muda mrefu, sasa wameweza angalau kuboresha sehemu ile, lakini tukumbuke ndani ya kilometa 35 hakuna udhibiti wowote. Niliwahi kusema hapa kuna ng’ombe wanavuka, wanapita ndani ya mpaka ule kwa siku siyo chini ya ng’ombe 200 au 300, Serikali inapoteza fedha pale, ningetamani kwenye bajeti ya Mheshimiwa Waziri aone namna ya kusaidia haya maeneo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme pia kwenye maeneo ya mnada wa upili kwenye maeneo ya mipaka kupitia Wizara ya Mifugo, nimekuwa nikisema vile vile zaidi ya kilometa 35 mpaka 40 ili uweze kutembea pako wazi, pale chochote kinafanyika, inawezekana ninavyozungumza kuna watu wanavusha mifugo, Serikali inapoteza mapato mengi sana pale, niombe sana nalo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kwenye suala la kulipa kodi, nimpongeze na nimshukuru Mheshimiwa Waziri kwa namna ambavyo ameona kwamba sasa vijana wote ambao wanafikisha miaka 18 waweze kuwa na TIN Namba. Nimekuwa nikisema hapa na ningetamani mwishoni nalo pia alitolee maelezo, tunazo Taasisi za umma ambazo zinadaiwa zaidi bilioni 78 na Wizara ya Ardhi kama kodi ya ardhi, hawana tofauti hawa watu na mwananchi mnyonge ambaye tunamwambia nenda kalipe kodi yako leo na wakati tunayo mataasisi ya umma, mashirika ya umma yanadaiwa zaidi ya milioni 78. Yaani kama ndiyo hivyo kama tunashughulika na mwananchi kumwambia nenda kalipe kodi, haya mashirika yetu ambayo tunayo zaidi ya 114, lini wanalipa hizo hela?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema nimpongeze Waziri namna alivyosema kwamba Wakurugenzi wa hizi Taasisi wawe wanaingia kwa kufanya interview, lakini naomba asiishie hapo tu, aende awaambie Mkurugenzi asiyeweza kulipa kodi ya Serikali kama ambavyo tunashughulika, wao ndiyo wanatakiwa wawe mfano, hawalipi zile fedha, matokeo yake ni kwamba, Wizara ya Ardhi kila mwaka ikipanga bajeti zaidi ya 35% ya bajeti ya Wizara ya Ardhi kwenye kodi ya ardhi inategemewa kupatikana kutoka kwenye mashirika ya umma. Halafu ndani ya 35% hayo mashirika hayalipi hiyo fedha, kwa hiyo namwomba Mheshimiwa Waziri aikazie hii, haya mashirika ya umma yanayodaiwa fedha za Serikali, walipe tusiwe tunakwenda tunamng’ang’ania tu mwananchi kulipa halafu tunayo mashirika ndani yetu na hayalipi kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho kwa umuhimu wake, niombe sana Mheshimiwa Waziri wanapopanga hii bajeti na wanapokwenda kutengeneza mipango waangalie mazao ya kimkakati ya kila mkoa. Nilikuwa naona hapa kwenye kilimo Mkoa wangu wa Mara kila nikiusoma sioni, nilikuwa natamani sana Mheshimiwa Waziri wa Kilimo alione hili, hatuna zao la kibiashara la kimkoa ambalo tunatakiwa litunyanyue sisi kama mkoa, tunaona mikoa mingine inavyokwenda, lakini Mkoa wa Mara hatujafika mahali tukaona namna gani Serikali imepanga mikakati ya kutengeneza zao la kibiashara na likasimamiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo maeneo mengi ya kiuchumi kama viwanda vimekufa, Bandari ya Musoma imekufa, tulitamani angalau na sisi kupitia kilimo tuone ni zao gani ambalo Wizara imefanya utafiti na twende kutoa elimu kwa wananchi ili angalau liwe ni zao la kutubeba watu wa Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya mchango huu, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa hesabu zilizokaguliwa za Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa Mwaka wa Fedha ulioishia tarehe 30 Juni, 2022 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, awali ya yote na mimi nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama ndani ya Bunge na mimi kutoa maoni yangu juu ya Taarifa tatu za Kamati zilizowasilishwa katika Bunge lako hili.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, nichukue nafasi hii kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kudumisha utulivu, amani lakini pia kwa kujituma na kuhakikisha tunapata fedha za miradi ya maeneleo zinakuja kwenye maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwanza kwa kumpongeza Mkaguzi na Mdhibiti wa Hesabu za Serikali kwa maana ya CAG pamoja na ofisi yake kwa uzalendo wake mkuu na namna ambavyo anawajibika kuhakikisha angalau anadumisha na kurudisha uzalendo na uimara katika fedha za Serikali kwenye miradi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, tunakubaliana kwamba Ofisi ya CAG kama Mdhibiti wa Hesabu za Serikali ametimiza wajibu wake. Mbele yetu sisi tunao mtego, sisi kama Bunge la watunga sheria ambao kimsingi yanayokwenda kukaguliwa na CAG na yanayotekelezwa na watumishi mbalimbali yanaendana na sheria mbalimbali ambazo zimetungwa ndani ya Bunge hili na sisi ndiyo watungaji wa sheria hizi.

Mheshimiwa Spika, mtego ulioko mbele yetu ni pale ambapo taarifa hizi zinakuja na baadhi yetu wataalam na watumishi mbalimbali wamekiuka sheria na taratibu mbalimbali ambazo zinatungwa ndani ya Bunge na sisi kama Wabunge tunaingia mjadala wa kuweza kuzijadili.

Mheshimiwa Spika, kwa kuendelea kutoa maoni ya Taarifa ya CAG ningetamani tutakapopata nafasi ya Waheshimiwa Mawaziri mimi ningependa sana nitoe ushauri, watakaposimama kwanza tupitie mapendekezo ya Bunge hili ya Taarifa ya CAG ya miaka miwili au mitatu iliyopita kabla hatujaanza kupitia mapendekezo ya mwaka huu.

Mheshimiwa Spika, kwa kufanya vile tutakuwa moja; tunadhibiti na kuimarisha maelekezo ya Bunge hili kwamba Bunge linapotoa mapendekezo ya kwenda kufanyiwa kazi basi uimara wa taarifa huo uweze kufanyika. Kwa mfano, wakati tunajadili mwaka jana Taarifa ya CAG ilionekana kwenye fedha za mikopo peke yake, mikopo ya vijana, wanawake na walemavu, taarifa ya mwaka jana kwa maana ya 2020/2021 zaidi ya shilingi bilioni 47 zilikuwa zimekwenda mahali ambapo kuna utata hazieleweki. Mwaka huu Taarifa ya CAG inazungumza zaidi ya shilingi bilioni 88 kwa maana hiyo zimeongezeka zaidi ya mara mbili na kwenyewe matumizi yake hayaeleweki.

Mheshimiwa Spika, kwenda kujadili shilingi bilioni 88 peke yake tukaacha kupata maelekezo ya Serikali na Wizara husika hatua walizochukua kwa Wakurugenzi, Maafisa Maendeleo na Wakuu wa Idara mbalimbali waliosababisha hasara ya shilingi bilioni 47 tunakoenda kujadili shilingi bilioni 88 maana yake tunaacha kiporo huku nyuma na inawezekana mwakani tukarudi tena kujadili zaidi ya shilingi bilioni 88. Kwa hiyo, uendelevu huu ni lazima tuhakikishe kwamba sisi tunausimamia.

Mheshimiwa Spika, la pili, kwenye Bunge hili tumetunga Sheria kwamba mwananchi akinunua chochote, akihitaji mahitaji yoyote au bidhaa yoyote ni lazima aombe risiti. Sheria hiyo tumekwenda kutengeneza Kanuni kwamba asipoomba risiti mwananchi mnyonge wa kule kijijini anatakiwa kulipa shilingi milioni tatu kwa ile risiti ambayo hakuomba. Hili limekuwa likifanywa na TRA na wenzetu na linasimamiwa ipasavyo.

Mheshimiwa Spika, sasa tujiulize sisi Serikali imefanya malipo ya zaidi ya shilingi bilioni 10 na hawajaomba risiti ya eletroniki, lakini wamelipa fedha. Sasa tunataka tujue nani anayewajibika hapa na ndiyo maana ninasema Waheshimiwa Mawaziri sisi inawezekana hatuna ubaya na ninyi tunataka tujue mtakavyokuwa mnatoa majibu hasa Waziri husika. Wakurugenzi wa hizi Halmashauri wote waliotoa risiti ambao kimsingi mmeshindwa kuwaomba ile shilingi milioni tatu ambayo mwananchi wa kawaida anatoa. Ukisimama kutoa majibu…(Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi jana Mawaziri walikuwa wanatoa taarifa sana kwa Waheshimiwa Wabunge, naomba na sisi uturuhusu leo Waziri atakapokuwa anatoa majibu ambayo hayaridhishi kwenye kipengele ambacho tunahitaji majibu tupe nafasi tumpige taarifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi ningetamani Waziri husika aniambie Wakurugenzi waliolipa fedha hizi bila risiti za elektroniki wako wapi na asiniambie wahewahamisha kutoka kituo “A” kwenda kituo “B.” Nataka aseme hadharani wamefukuzwa, wako kwa mujibu wa sheria mahakamani au wako wapi. Ukiniambia umewatoa sehemu “A” kwenda sehemu “B” nitaomba unipe nafasi ya kum-correct Mheshimiwa Waziri huyo ili angalau twende sawasawa. Kwa kufanya hivyo tutakuwa angalau tunakwenda kama vile inavyotakiwa.

Mheshimiwa Spika, la pili, Mheshimiwa Waziri husika atakaposimama leo atuambie leo ndani ya Bunge fedha ya POS ambayo imekusanywa shilingi bilioni 11 hazikupelekwa benki, hizi fedha hawa Wakurugenzi na Wakuu wa Idara wamezipeleka wapi? Aseme yeye yaani natamani jibu liwepo kwamba hawa Wakurugenzi wa hizi Halmashauri waliosababisha upotevu wa fedha hizi leo watatu wako mahakamani, wanne wako sehemu fulani na usiniambie umewahamisha kutoka sehemu “A” kwenda sehemu “B.”

Mheshimiwa Spika, inauma sana na naamini wote tutakubaliana, ni sawa na mtu una duka lako umemuweka kijana asimamie mauzo ya duka lako, halafu yule kijana anakuibia fedha ya kwako wewe mfukoni. Anachokiuza anakipeleka mfukoni hapeleki benki wala hakupi wewe eti kwa kujifurahisha na kuchukua hatua unamhamisha kutoka kwenye duka “A” unampeleka kwenye duka “B” halafu unapiga makofi kwa kujipongeza kwamba nimechukua hatua zinazostahili, hii si sawa.

Mheshimiwa Spika, maana yake ni kwamba kama wewe una uchungu na yule kijana aliyekuibia fedha yako maana yake utachukua hatua stahiki. Tunataka tuone Waheshimiwa Mawaziri mtakapokuwa mmesimama kutoa taarifa hapa mtuambie hawa Wakurugenzi na Wakuu wa Idara mmechukua hatua gani za kinidhamu? Hili nadhani litaongeza umaarufu.

Mheshimiwa Spika, pia natamani nitoe ushauri kwa Mheshimiwa Waziri na kwa Serikali kwa ujumla wake. Haya yote yanafanyika kwa sababu ya sheria zilizopo, Sheria ya Utumishi wa Umma, sheria mbalimbali za usimamizi wa manunuzi na sheria zote zinazoendesha miradi ya maendeleo.

Mheshimiwa Spika, naomba Mheshimiwa Waziri aone namna ya kurekebisha hizi sheria. Kwa mfano, leo kijana analipwa mshahara wa shilingi 800,000 mpaka shilingi 1,000,000, afisa wa kawaida. Shilingi milioni moja au laki nane kwa mwezi kwa mwaka maana yake anachukua milioni kumi huyu kijana. Kwa miaka mitano ukizidisha shilingi milioni kumi maana yake ana shilingi milioni hamsini peke yake, kwa miaka kumi ndiyo ana shilingi milioni 100. Amekutana na deal la shilingi bilioni mbili mezani kwake ambayo akifanya kazi ya utumishi wa umma kwa zaidi ya miaka 30 hata 50 mpaka anastaafu hawezi kupata ile shilingi bilioni mbili maana yake atakupiga shilingi bilioni mbili na akikupiga shilingi bilioni mbili anajua sheria yenyewe iko weak. Kwa sababu sheria yenyewe ni kwamba utamsimamisha, utamchukua utampeleka TAKUKURU, utampa barua ya kujieleza, ndivyo zinavyozungumza maana yake huyu hawezi kuogopa kuiba fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nikaishauri Serikali ifanye mabadiliko ya sheria na ndiyo maana jana tulisema hapa ikibidi iseme mtu wa aina hii kama siyo kunyongwa basi itamke kitu ambacho kinaweza kikafanya watu wote wakaweza kuogopa kuchezea fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, lingine ni TAKUKURU; nataka nijue ni chombo gani kinachowasomamia TAKUKURU? Leo Mkuu wa Wilaya akienda kukagua miradi akikuta kuna ubadhirifu utasikia anasema hili liende TAKUKURU. Mkuu wa Mkoa hivyo hivyo akija Waziri hivyo hivyo, akija Waziri Mkuu hivyo hivyo; najiuliza TAKUKURU ukiacha haya ambayo yametajwa humu kwenye Taarifa ya CAG haya ambayo yanatolewa matamko na viongozi wa kisiasa na viongozi wa Serikali TAKUKURU anayo mangapi?

Mheshimiwa Spika, nani anaki-regulate kile chombo kuhakikisha haya maelekezo, hizi kesi mbalimbali TAKUKURU anazipeleka mahakamani na zinafanyiwa kazi? Nani anaye-regulate? Ndiyo maana ukiangalia hii Taarifa ya Kamati wanasema TAKUKURU ni kichaka cha taarifa mbalimbali kwa sababu hakuna chombo na kama kipo maana yake kimeshindwa kusimamia TAKUKURU kuhakikisha kesi mbalimbali zinakwenda mahakamani.

Mheshimiwa Spika, ndiyo maana tunashauri kiwepo chombo maalum ambacho kinafuatilia kesi mbalimbali zote na matamko ya wanasiasa ambayo TAKUKURU wanapewa jukumu lake ili angalau kila mwezi kwa miezi mitatu tupate taarifa kwamba wanachukua hatua gani juu ya utekelezaji wake.

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Jafari Chege kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Getere.

TAARIFA

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Spika, nilitaka kumpa taarifa kwamba baada ya Wilaya ya Bunda kupokea kesi zaidi ya 40 za TAKUKURU nilipoenda kwa TAKUKURU Wilaya akasema yeye hana uwezo wa kupeleka hao watu mahakamani mpaka apate idhini ya TAKUKURU Mkoa, kwa hiyo ni process. (Kicheko)

SPIKA: Mheshimiwa Jafari Chege unaipokea taarifa hiyo?

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa ndiyo maana nikashauri kwamba kiwepo chombo ambacho kinawa-regulate, kinawa-control hawa watu. Kwa sababu TAKUKURU ukiacha kesi ambazo zimetajwa kwenye taarifa wewe ni shahidi haiwezi kupita mwezi hujasikia viongozi wa kisiasa au Kiserikali kusema jambo hili, kama imetokea mradi wowote wa wananchi, jambo hili TAKUKURU chukua ukalifanyie kazi. Nani anayeyafuatilia yale mambo kama yanafanyiwa kazi sawa sawa ili mwishoni angalau Wabunge au Serikali au wananchi wote tupate taarifa sahihi kwamba kesi hizi zinakwenda inavyotakiwa. (Makofi)

SPIKA: Haya ahsante sana kengele ya pili ilikuwa imeshagonga.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika nakushukuru sana. Naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushuru kwa kunipa nafasi. Kabla sijasahau kwanza nianze kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa kazi kubwa ambayo wamekuwa wakiifanya.

Mheshimiwa Spika, nami niendelee kusisitiza kwamba Giza Cable Industry huyu mkandarasi ambaye amepewa kazi katika Wilaya nne za Tarime, Serengeti, Butiama pamoja na Rorya, mkandarasi huyu kama alivyosema Mheshimiwa Sagini hapatikani kwenye simu. Sisi kama wakazi wa Mkoa wa Mara kwenye hizi wilaya nne tunapata wasiwasi kwa sababu kama wakandarasi wengine wamekwishaanza kufanya survey lakini yeye mpaka sasa hapatikani. Leo asubuhi nilikuwa naogea na Injini wa Wilaya yangu Rorya anasema hajaona mkandarasi yeyote maeneno yale. Kwa hiyo, kama Bwana Giza ananisikia popote alipo basi ni vema tukafanya mawasiliano ili angalau atuondoe kwenye adha hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya utangulizi huo, naomba nishauri mambo mawili ambayo yako ndani ya jimbo langu. La kwanza ni kushukuru kwa kazi kubwa iliyofanyika katika Jimbo langu la Rorya, ndani ya vijiji 87 vijiji 73 vyote tayari vina umeme wa REA. Ni imani yangu kwa Vijiji 14 vilivyobaki vya Kanyamsana, Kabache, Nyamusi, Masike, Nyabikondo, Burere, Wamaya, Nyabihwe, Nyihara, Bugendi, Busanga, Ulio, Tai pamoja na Lalanya navyo vitapata umeme. Ni imani yangu utekelezaji wa REA awamu hii vijiji vyote vitakuwa vimepata umeme.

Mheshimiwa Spika, ni imani yangu Mheshimiwa Waziri atatusaidia pia kutatua kero kwenye maeneo ambayo tayari ndani ya vijiji 73 hivi ambavyo umeme umefika ili angalau maeneo mengine waweze kupata umeme. Kwa sababu hiyo Mheshimiwa Waziri nishauari maeneo mawili, ni kweli umeme umefika kwenye vijiji 73, lakini kwenye kijiji kuna kaya au wakazi wako 20 kwenye center ya Kijiji, unaweza ukaona kwamba kama wako watu 20 ni nyumba tano tu ndizo zinazopata umeme lakini nyumba 15 hazina umeme. Sasa kwa status ya Rorya jinsi ilivyo katika hizo 15 bado unakuta watu 10 tayari wamelipia umeme zaidi ya mwaka mmoja lakini hawajaunganishiwa umeme. Kwa hiyo, unaweza ukaona kwamba wananchi wengi pamoja na kwamba tunawaambiwa ndani ya kijiji chenu wana umeme hawaoni tija ya umeme ule.

Mheshimiwa Spika, atakuambia tu Mheshimiwa Mbunge ninachoona ni nguzo mimi nimelipia nina miaka miwili au mwaka mmoja sijapata huo umeme. Zile kaya tano zilizosalia wanashindwa kulipia kwa sababu wanaona wenzao mpaka sasa hawajatatuliwa tatizo lolote la umeme. Nikuombe Mheshimiwa Waziri kipindi unakimbizana na namna ya kutatua changamoto ya vijiji vilivyosalia nchi nzima tupeleke fedha TANESCO ili wakimbizane kumalizi hivi vijiji vilivyosalia ili hawa watu 15 waliosalia na waweze kupata umeme katikati ya kijiji kwenye maeneo ya centre. Kwa kufanya hivyo utakuwa umetatua tatizo zima la eneo lile.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili nizungumzie kuhusu kukatikakatika kwa umeme. Mimi kwangu ni changamoto kubwa sana, naweza nikawa naongoza kwenye Mkoa wa Mara kwa Jimbo la Rorya kukatika umeme. Changamoto kubwa ni ukubwa wa kilometa za mraba ambazo TANESCO Halmashauri ya Wilaya ya Rorya wanazohudumia. Watu hawa wanahudumia zaidi ya kilometa 344, kutokea Nyamongo mpaka ndani ya jimbo zima ni zaidi ya kilometa 344.

Mheshimiwa Spika, lakini ukifuatilia historia ya umeme ule nguzo zina zaidi ya miaka 40 kwa hiyo zimechoka na kuchakaa. Pamoja na kwamba utakuja kutoa majumuisho na kutoa mwelekeo wa nchi nzima ni kwa nini umeme unakatikatika lakini solution kubwa ni kupeleka fedha za kuboresha miundombinu kwenye maeneo haya. Hizi nguzo za umeme zina miaka 40 sasa kwenye maeneo ambayo kuna chemchem zinaoza halafu zinadondoka ndiyo maana mpaka leo ninavyozungumza kuna maeneo ndani ya jimbo langu watu wana siku tatu hawana umeme. Hivi ninavyozungumza kuna Kijiji cha Chabakenye toka jana mchana hakuna umeme wowote lakini ukifuatilia unakuta miundombinu hii imechakaa.

Mheshimiwa Spika, kwa namna yoyote hata kama Mheshimiwa Waziri atafanya marekebisho ya watendaji mimi niseme kwamba inawezekana hawana wakawa hawana kosa. Kikubwa ambacho anaweza kufanya ni kupeleka fedha ya miundombinu hasa fedha maintenance kwenye maeneo haya ambayo umeme unakatika mara kwa mara. Pamoja na kwamba atakuja na suluhisho lingine lakini aamini nachosema umeme huu kwa maeneo haya nguzo zina muda mrefu sana toka zimeoteshwa. Akitatua hilo pamoja na mengine atakayokuja nao naamini kwenye halmashauri hizi ambazo ziko pembezoni atakuwa amewaokoa kwa kiwango kikubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami nianze kwanza kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa na nzuri aliyoifanya kwenye majimbo yetu, na pia kwa kukubali na kuridhia kuinua sekta ya Wizara hii ya Kilimo kwa kuiongezea fedha. Nichukue nafasi hii kuwashukuru sana Mawaziri, watendaji wote, hasa Mkurugenzi wa Tume ya Umwagiliaji, ndugu yangu Raymond Mndolwa kwa namna ambavyo amejikita kuhakikisha angalau skimu mbalimbali ambazo zilikuwa ni mapendekezo ya Bunge zinaweza kufanyiwa kazi na zinatengewa fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizi kipekee nichukue nafasi hii kukushukuru sana Mheshimiwa Waziri, nimeona kwenye bajeti ya mwaka huu, zipo schemes za wilayani kwangu Wilaya ya Rorya, kwa muda mrefu tumekuwa tukiziombea ziingie kwenye mpango mkakati na umeezingiza. Ikiwemo scheme ya Rabong nichukue nafasi kukushukuru, ikiwemo Chereche, Ryangubo, Rwang’enyi pamoja na scheme ya Mto Mara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na shukrani hizi Mheshimiwa Waziri, yapo mambo ambayo ningetamani nishauri kwa maana ya Mkoa wetu wa Mara. Mheshimiwa Waziri, utakubaliana na mimi pamoja na kwamba Mkoa huu ndio Mkoa anaotoka Muasisi wa Taifa hili, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, pamoja na kwamba mkoa huu ndio anaotoka Muasisi aliyekuwa anaAsisi sekta na Wizara unayoiongoza ya Kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia utakubaliana na mimi kwamba Mkoa wa Mara ukiuzungumzia kwa sasa ni mkoa ambao hauna zao la kimkakati, hauna zao la kibiashara na ni mkoa ambao hata mazao yanayolimwa ya chakula haya- sustain. Ni mazao ambayo yanalimwa kwa ajili ya chakula cha kujilisha wenyewe na sio mazao yanayokwenda kwenye sekta kwa maana ya kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nimekuwa nikishauri hapa ndani ya Bunge, sio kwamba tunapungukiwa baadhi ya mambo yanayoweza kutufanya na sisi tukawa na mazao ya kimkakati na mazao ya kibiashara kama ilivyo mikoa mingine. Nadhani ni uamuzi wa Wizara na intervention ya Serikali a very serious interventions ambayo inaweza ikatusaidia sisi kama mkoa kutupa direction ya namna njema ya kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Mara utakubaliana na mimi Mheshimiwa Waziri, tuna zaidi ya hekta milioni mbili lakini tunazalisha hekta laki mbili mpaka laki tatu peke yake. Mazao tunayolima mengi yao ni mahindi na tukilima yale mazao ni mazao ya chakula peke yake. Hatulimi mazao kwa ajili ya kufanya kwa maana ya kujiinua kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia utakubaliana na mimi ni mkoa ambao tuna irrigation scheme zaidi ya 42, lakini zinazofanya kazi hazifiki hata 10 peke yake. Ni mkoa ambao umezungukwa na ziwa, kwa mfano wilayani kwangu asilimia 77 nimezungukwa na ziwa lakini hakuna mazao yanayolimwa ambayo unaweza ukasema haya ni mazao ya kibiashara ya kumkomboa mwananchi kwa ujumla wake na yakatangaza ule mkoa kibiashara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe Mheshimiwa Waziri, katika ziara hizi unazozunguka, kwanza upe Mkoa wa Mara kipaumbele, tengeneza a very serious intervention ya kuja kwenye Mkoa wa Mara na kutengeneza ushauri kuona namna unavyoweza kukaa na wadau wa sekta ya kilimo na wananchi wanaofanya shughuli za kilimo ili kuinua mazao ya kibiashara ili leo tunaposimama sisi kama mkoa tuwe tuna zao la kibiashara tunalotambua kama mkoa, kuwe kuna zao la kimkakati lakini pia utengeneze strategies nzuri ya kuona namna unavyoweza kuwakwamua wakulima hawa wanaolima mazao madogo madogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niombe sana Mheshimiwa Waziri, hili ulione kwa jicho pana sana. Kwa sababu ukanda ule sisi Mkoa wa Mara ndio maana unaona hakuna tunachoweza kusimama. Siwezi kuzungumzia mbolea, siwezi kuzungumzia pembejeo na wakati hata kilimo kinachofanywa bado ni kidogo sana. Tunafanya small scale agriculture ambayo tungeweza kufanya large scale ili wananchi waweze kunufaika. Sasa nikuombe kwa kuwa umeanza kuzunguka maeneo mengi na haujafika Mkoa wa Mara, nikuombe uje in a very serious ili tukae tuweze kuona namna ambavyo tunaweza Kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba unafanya haya nikuombe Mheshimiwa Waziri, la kwanza kwenye zile scheme 46 pamoja na kwamba naona zimetengwa fedha lakini bado hazizidi scheme 10, nenda uone namna ambavyo zile scheme zote arobaini na kitu unavyoweza kuzipa fedha ziweze ku-produce ili wananchi waanze kulima kilimo cha biashara. Naona sasa scheme zinatumika kulima kilimo cha chakula peke yake. Pia, haya unayaweza naona maeneo mengine umekuwa ukifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, uone namna ya kutengeneza mahusianao mazuri ya private sector ili ziweze kuwekeza kwenye mazao ambayo yanweza yakai–boost kutenegeneza mazao ya kimkakati na mazao ya kibiashara na hili unaliweza kama ambavyo umekuwa ukifanya mikoa mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatu, utengeneze Mkoa wa Mara kuwe kuna soko rasmi la kuuza bidhaa. Leo sisi tunauza bidhaa zetu kwenye magulio na haya masoko ya kawaida. Hatuna soko rasmi ambalo wananchi wanauza bidhaa ambalo lita–motivate wananchi kuzalisha zaidi wakijua kuna mahali pa kuuza. Leo wakizal;isha inabidi wavuke waende Kenya kutafuta soko ambalo linaweza likawanufaisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani sisi kama mkoa ungeweza kutengeneza namna nzuri ya kutengeneza soko zuri moja wapo katika ukanda ule. Kwa bahati nzuri ukanda wote wa ziwa hakuna soko kubwa ambalo linauza mazao ya chakula kwa ujumla wake. Ona namna mkoa ule kwa sababu uko mpakani uweze kutusaidia tuweze kupata masoko mazuri ya kuuza bidhaa hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la nne, utakapokuwa umekuja ona namna ambayo tupate ghala la chakula ambalo litawafanya wakulima badala ya kuuza bei ya chini mazao yao wanapolima, waweze kuhifadhi wakisubiri bei nzuri ili na wao waendelee kutengeneza motivation. Pia, ninaamini kwa kufanya hivi utaweza kuwa motivate wakulima wengi pamoja na vijana ambao kimsingi wameamua kujiajiri kwenye sekta ya kilimo lakini hawana uwezo na hawana soko la uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine Mheshimiwa Waziri in a very serious kama nilivyosema, lazima utakaposimama hapa…

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. JAFARI W. CHEGE:… leo utuambie katika ukanda ule ni zao gani la kibiashara ambalo umeweza kuainisha na zao la kimkakati kwenye mkoa mziama wa mara. Tunayo mazao tunayolima ambayo yanakubali ardhi ya upande ule, Kahawa inakubali, tumbaku inakubali, mkonge unakubali. Pamba imekuwa ikilimwa kwa muda mrefu na wewe ni shahidi, lakini haya mazao haya yamekufa kwenye Mkoa wa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, yaani tukianza kuzungumza Mkoa wa Mara, hakuna zao tunalosimama nalo kama Mkoa. Sasa hatuwezi kwenda kwa style hii. Kama nilivyosema ni mkoa anaotoka muasisi ningetamani unavyosimama na wewe Mheshimiwa Waziri, ujivunie Wizara unayoiongoza muasisi wa sekta uya kilimo ni Mwalimu Nyerere. Kwa hiyo, sisi tungeona Mkoa wa Mara, unatunyenyuaje kwenye sekta ya kilimo, kwenye maeneo yote na sio hivi tunavyozalisha kwenye mazao ya chakula peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazalisha mahindi tani laki mbili mpaka laki tatu kwa mwaka na wakati mahitaji ni zaidi ya tani 600,000 mpaka 700,000. Kwa hiyo, hata hiyo nusu yenyewe hatufiki hata hilo zao moja lenyewe hatuwezi kufika. Kwa hiyo, nikuombe Mheshimiwa Waziri,...

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. JAFARI W. CHEGE:…utakapokuja kusimama jioni hapa uweke mpango mkakati wa namna utakavyokuwa kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, nakushukuru sana naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuwa mchangiaji wa kwanza jioni ya leo.

Mheshimiwa Spika, niseme tu kwamba leo nimesimama, sitakuwa na mambo mengi zaidi ya kutoa shukrani zangu za dhatii kwa niaba ya wananchi wa Rorya, kwanza kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan, pili, kwa Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii pamoja na Manaibu wake wawili, hasa Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Kasekenya. Pia nitoe shukrani zangu za dhati kabisa kwa Watendaji kwa maana ya Makatibu Wakuu wa Wizara hii hasa Dada yangu Ndugu Aisha, pia nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Meneja wa TANROADS Mkoa wa Mara.

Mheshimiwa Spika, nimeanza kutoa pongezi hizo kwa kipekee kabisa kwa niaba ya wananchi wa Rorya kwa Serikali hii ya Mama Samia kuridhia maombi zaidi ya miaka 40 ya barabara ambayo tumekuwa tukiiomba muda mrefu hapa ya lami kutoka Mika – Utegi – Shirati mpaka Mpakani mwa Kenya Kirongwe kuingizwa kwenye mpango wa bajeti kwa ajili ya ujenzi wa lami.

Mheshimiwa Spika, naomba niwashukuru wananchi wangu na kwa kuwa wananisikia na waliniambia nifikishe salamu na pongezi hizi na shukrani za dhati kabisa kwa sababu barabara hii siyo tu kwamba ni barabara ambayo inatuimarisha usalama kati ya nchi na nchi, lakini ni barabara ambayo ikijengwa kwa kiwango cha lami inakwenda kuinua uchumi wa Halmashauri yenyewe, uchumi wa Mkoa wa Mara, lakini uchumi wa Serikali kwa ujumla kwa sababu inakwenda kugusa nchi mbili.

Mheshimiwa Spika, mbali ya hivyo, hii ni barabara ambayo kimsingi tumeiomba kwa muda mrefu sana. Ilani ya Chama cha Mapinduzi toka mwaka 2010 ilikuwa inasemwa barabara hii itaingizwa kwenye mpango wa utekelezaji lakini ilikuwa haifanyiki, toka 2005, 2010 mpaka leo kwa Awamu hii ya Sita angalau imeweza kuingia kwenye mapendekezo ya ujenzi wa lami.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri na Serikali kwa ujumla kwa maana ya Wizara hii, niombe sasa kwa kuwa tayari imekwishaingia kwenye mpango wa utekelezaji wa lami, iweze kutengewa fedha, kwanza itangazwe lakini itengewe fedha ambazo itaweza kujengwa kwa kilometa zote 56. Ninaamini wananchi wamefarijika sana na ndiyo furaha yao kubwa.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili nataka tu nimkumbushe Mheshimiwa Waziri, kama nilivyosema leo mimi sina mambo mengi kwenye Wizara hii, kwa furaha tulizonazo sisi tunaamini kabisa kwamba wananchi wote katika Wizara hii wamefarijika sana. Natamani nimkumbushe Mheshimiwa Waziri juu ya Kivuko cha MV Musoma. Kwa kuwa kivuko hiki kilikwenda kwenye matengenezo, mara nyingi Mheshimiwa Waziri nimekuwa nikikuuliza ndani hapa, kwenye majibu ya nyongeza umekuwa ukitoa ahadi kwamba angalau kile kivuko, mwanzoni ulisema tarehe 30 Aprili kitarejea na kitaanza kutoa huduma.

Mheshimiwa Spika, siyo hivyo tu, Kiongozi kwa maana ya Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama, Mwenyekiti wa Umoja wa Wazazi Taifa, naye alipokuwa katika eneo lile alikupigia simu ukaahidi kile kivuko kitarudi kabla ya tarehe 05 Aprili. Leo ni tarehe
23 Mei, Mheshimiwa Waziri ninatamani wakati unafanya majumuisho, wale wananchi wanaotumia kivuko kile wangetamani wapate kauli yako, ni lini kile kivuko kinarudi kwa ajili ya kutoa huduma kwa kuwa kile kivuko kilichopo ni kidogo na siyo salama kwa maisha yao.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la tatu ambalo ninatamani pia nikukumbushe ni juu ya bandari ya Musoma. Nimeona kwenye hotuba yako Mheshimiwa Waziri, zipo bandari kadhaa ambazo zinakwenda kufanyiwa matengenezo, bandari za Mwanza na maeneo mengine, lakini sijaiona bandari ya Musoma ikitajwa.

Mheshimiwa Spika, nilichangia mwaka jana kwenye hotuba ya bajeti ya Wizara yako na nikakuomba sana kwa unyenyekevu mkubwa, bandari ile sisi kwetu ndiyo kiungo muhimu cha kuinua uchumi wa Mkoa wa Mara. Nasi Mheshimiwa Waziri wewe ni shahidi, ile bandari imesahaulika kabisa. Kwa sasa ilivyo imechakaa na haifai. Ninaomba sana kwenye bajeti hii, pamoja na kwamba tayari mmetaja bajeti zingine, muone namna ya kuifufua ile bandari.

Mheshimiwa Spika, kwetu ile bandari ndiyo kiungo muhimu cha kuinua uchumi wa Mkoa ule wa Mara. Lakini sisi tunaitegemea ile bandari iweze kufanya kazi, kwa sababu tunayo bandari ya Sota eneo la Rorya ndiyo muunganiko wa bandari zote mbili. Kwa kuwa Mheshimiwa Waziri kwenye bajeti na utekelezaji kwenye hotuba yako umesema hapa tunajenga Reli ya SGR, matarajio yetu ni kwamba reli ya SGR baada ya kuwa inafika Mwanza, tunatamani kutokea Mwanza kwenda maeneo mengine kwa maana ya Nchi za Kenya na Uganda, waweze kutumia bandari ya Musoma, waweze kutumia bandari ya Sota kufika maeneo ya Kenya na Uganda. Sasa isipokuwa inawekwa kwenye bajeti kila mwaka inakuja haitengewi fedha na ilivyochakaa pale Mheshimiwa Waziri, haipendezi. Ninatamani sana na yenyewe muiweke kwenye vipaumbele Bandari ya Musoma Mjini na Bandari ya Sota. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho kama nilivyosema, ni juu ya jengo la abiria kwenye eneo la kivuko cha Musoma na upande wa Kinesi. Wananchi wale wakati wa mvua na wakati wa jua kali Mheshimiwa Waziri, hawana mahali pa kujikinga jua wala mvua wakiwa wanasubiri kivuko. Ninaomba pia, nimeona kwenye bajeti umelisemea, kivuko hiki kiharakishwe kwenye pande zote mbili, upande wa Kinesi na upande wa Musoma ili angalau kuweza kurudisha matumaini na kuweza kuwasaidia hawa wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri, nimeona hapa Barabara ya Kuruya – Makutano kwa maana ya Makutano – Komuge mpaka Kinesi mmeiweka kwenye utekelezaji kwa ajili ya kuandaa mpango kwa maana ya ufanisi. Ninaomba barabara hii pia kwa bajeti ya mwakani tuiwekee lami kwa sababu ni muhimu sana kiunganisho kati ya maeneo ya kivuko, maeneo ya Kinesi na upande wa Kuruya kuja maeneo ya Musoma mpaka Mwanza. Kwa kuwa mmetenga fedha za upembuzi yakinifu, ninaomba sana mwakani Mheshimiwa Waziri barabara hii pia uikumbuke.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyosema mimi kwenye Wizara hii sikuwa na neno kubwa zaidi ya kutoa shukrani kwa furaha kubwa ambazo wananchi wangu wamefarijika. Nitumie nafasi hii kukuomba sasa Mheshimiwa Waziri usiishie tu kuiweka kwenye bajeti, barabara hii ni muhimu sana kwa kiungo cha Mkoa mzima wa Mara iwekee fedha itangazwe ili ianze kujengwa kwa kiwango cha lami kwa maana ya kutoka Utegi – Shirati kwenda mpaka kule Sota na maeneo ya Kirongwe. Ninaamini kabisa itafungua uchumi wa hizi Nchi mbili kwa maana ya Kenya na Tanzania.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi, ahsante sana. naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi na mimi awali ya yote kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu Wataallah kwa kunipa afya njema na kunijaalia leo angalau na mimi nimesimama kuweza kuchangia bajeti hii ya Wizara ambayo kimsingi ndiyo kichocheo cha uchumi wa maeneo mengi nchini kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kabla sijaanza mchango wangu nichukue nafasi hii pia kumshukuru Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa namna masikini ya Mungu ambavyo kila kukicha anahangaika kutafuta pesa mahali pole ndani na nje ya nchi ili kuweza kunusuru shughuli za kimaendeleo na shughuli kubwa ambazo zinachochea uchumi wa nchi yetu kwa ujumla wake. Hopeful na sisi tutaendelea kumuombea Mwenyezi Mungu aendelee kumpa afya njema, aendelee kumfanya awe mvumilivu na aendelee kuchapa kazi tukiamini kabisa lengo lake na nia yake ni njema kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nitachangia maeneo matatu; la kwanza nitachangia umuhimu wa Wizara hii katika uchocheo wa uchumi wa nchini kwetu. Mimi ninavyojua Wizara hii ni kama catalyst ndio maana ukiona vipaumbele vingi ambavyo vinachochea ukuaji wa uchumi kwa maana ya bandari, barabara, vivuko na maeneo mengine yapo ndani ya Wizara hii. Kwa maana ya kwamba bila Wizara hii kufanya kazi inavyotakiwa basi ninaamini kabisa uchumi endelevu wa nchi na maeneo mengi hautafikiwa kwa wakati wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili ndilo ambalo linanifanya leo nielekee kwenye mchango wangu na natambua kabisa nje ya human resource, nje ya natural resource pamoja na political stability lazima infrastructure za nchi ili uchumi wake uweze kukua kwa haraka lazima infrastructure ziwe stable, ziwe nzuri, kuwe kuna connection kati ya Mkoa mmoja na Mkoa mwingine, kuwe kuna connection kati ya Wilaya watu waweze kuwasiliana, lakini ikibidi kuwe kuna connection kati ya nchi na nchi. Sasa hili la nchi na nchi ndiyo linanipelekea mimi kuchangia barabara yangu ya Utegi - Shirati na Kirongwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa Kirongwe ni mpakani mwa Kenya na Tanzania na nimekuwa nikisema sana. Kwa bahati mbaya sana Mheshimiwa Waziri wewe ukiwa Waziri wa Maji ulipita barabara hii unaifahamu. Mwaka 2020 Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa kwenye kampeni na mimi nimshukuru sana kwa namna ambavyo alikuwa amejitoa, aliahidi barabara hii kwa maana ya kutoka Mika - Shirati mpaka Kirongwe zaidi ya kilometa 44 na kilometa 12 jumla ni kilometa 56.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama toka mwaka 2005, 2010, 2015, 2020 inataja barabara hii. Mheshimiwa Rais tarehe 5 Februari, 2022 alivyotembelea ndani ya mkoa nilivyopata ridhaa mimi na Mwenyekiti wa CCM Mkoa na viongozi wengine tulizungumzia barabara hii, unaifahamu kinaga ubaga. Sasa cha kushangaza ni kwamba na hata humu Waheshimiwa Wabunge mimi nilivyoingia mwaka 2020 nilikuwa ni mtu wa kwanza kuulizia utengenezaji wa hii barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wa Viti Maalum mbalimbali wamekuwa wakisimama ndani ya Bunge wanauliza barabara hii. Cha kushangaza na kinachoniumiza zaidi ni kwamba pamoja na maulizo yote hayo humu ndani bado unaendelea kutenga fedha ya ujenzi wa mita 500 peke yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ile ina urefu wa kilometa 56 mpaka Kirongwe mpakani kwa umuhimu wake, umuhimu wa Tanzania na Kenya kila mwaka mnatenga mita 500, mita 700 maana yake mpaka tufike mpakani tunahitaji zaidi ya miaka 50 ili kutimia kule maana yake hata mimi Mheshimiwa Mbunge sitakuwepo na wengine hawatakuwepo ndiyo tunafika mpakani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nadhani watu ambao wanaandaa hizi barabara za kimkakati wawe wanaangalia umuhimu wa barabara kwenye uchumi na ukuaji wa uchumi ili wapeleke fedha badala ya kila mwaka tunarudi tunatenga fedha kwenye kurekebisha na kutindua barabara kama Mheshimiwa Mbunge aliyepita alivyotangulia kusema. Tunashindwa kuweka vipaumbele kwenye barabara mpya zinazotuunganisha kati ya nchi na nchi, mkoa na mkoa ambazo tunazijua kabisa hizi barabara zikitengenezwa zinakuza uchumi wa nchi ile lakini pia zinakuza uchumi wa wananchi hawa ambao wanazunguka maeneo hayo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba sana Mheshimiwa Waziri utakapokuja hapo kesho kufanya majumuisho, kwa sababu unaifahamu barabara hii waambie wananchi wa Rorya ni lini barabara hii itajengwa. Cha ajabu zaidi ambazo mimi nimekuwa nikiumia, mwaka jana wametenga mita 700 hivi ninavyozungumza kwa bajeti ya mwaka jana 2021/2022 hakuna mkandarasi yeyote ambaye yuko site. Hata hizi mita 500, mita 700 mnazoweka hakuna mkandarasi site. Sasa leo tena umetutengea mita 500, mimi najiuliza hii accumulation ya mwaka jana na ya mwaka huu itajengwa lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama bado tunaomba kilometa 56 hazijawezekana, leo tunatengewa mita 500 na hakuna mkandarasi site, inaumiza sana. Nikuombe Mheshimiwa Waziri utakapokuja kwa sababu barabara hii unaifahamu, wananchi wasikie barabara ya Mika-Shirati kwenda Kirongwe ambayo ndiyo msingi wa kuunganisha kati ya hizi nchi mbili inajengwa lini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili siyo barabara hii peke yake, kKilichoniuma ni kwamba sisi ndiyo tunaopakana na Kenya. Ukitoka Sota ukipita zile Kata za Roche, Golibe mpaka Ikoma inapakana na Tarime Vijijini ni mpakani. Hapo ulipokaa Mheshimiwa Waziri na hapa nilipokaa, hapo ulipokaa ni Kenya hapa ni Tanzania katikati ndiyo kuna barabara. Barabara ile sikuiona ikiwekwa kwenye bajeti wala sikuiona inatengewa fedha yoyote wala sikuona inazungumzwa na ndiyo barabara inayotuunganisha sisi Wakenya na Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu ukienda upande wa pili Mheshimiwa Waziri wewe ni shahidi, kule wameanza kujenga barabara zao zinazowaunganisha kutoka Kenya kuja Tanzania, sisi hata fedha tu ya feasibility study kwenye hizi barabara hamna.

Sasa mimi nikuombe Mheshimiwa Waziri vipaumbele vingi kwenye barabara hizi ziende kwenye barabara ambazo zinaweza kukuza uchumi kati ya nchi na nchi, lakini zinakuza uchumi kati ya mkoa na mkoa kwa sababu sisi bidhaa yetu watu ambao wananunua bidhaa wengi wanatoka Kenya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunategemea kwamba kuwe kuna miundombinu imara maana yake sisi uvuvi ambao tunavua na kwa asilimia kubwa tunachofanya shughuli yetu ya kiuchumi, tunafanya shughuli ya kilimo pamoja na mifugo, watakuja Tanzania wakiwa wanaamini kabisa miundombinu iko imara. Nikuombe sana vipaumbele hivi kama ambavyo nimeona Mkurugenzi wa Bandari anahangaika kutafuta watu wengine waweze kuvusha biashara bandari. Ningetamani watu wanaohusika na barabara pia wanapotenga bajeti zao waweze kuainisha barabara za kimkakati ambazo zinaweza kukuza uchumi wa nchi kwenye maeneo yote nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili Mheshimiwa Waziri nichangie kwenye kivuko; hiki kivuko kinachoitwa cha Musoma – Kinesi asilimia 70 ya wananchi wanaokuja Musoma wanatoka jimboni kwangu, Tarafa ya Suba, Tarafa ya Loimbo, Tarafa ya Nyanje; yaani kile kivuko kwa namna moja ama nyingine kinawahudumia sana wananchi wa Wilaya ya Rorya. Hakuna sehemu unapata mahitaji kwa sababu mji uliokuwa kwenye Wilaya ya Rorya ni Musoma na ili tuje Musoma ni lazima tuvuke kupitia kivuko hiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa unaweza ukaona population ya watu zaidi ya 50,000 wanategemea kivuko hiki ili kupata mahitaji yao Musoma Mjini. Leo ninavyozungumza na wewe kivuko kilichopo ambacho kilikuwa kinatoa huduma hii mmekitoa kimepelekwa kwenye matengenezo. Kilichobaki ambacho mmekileta ni kidogo sana, inafika mahali Mheshimiwa Waziri kile kivuko kama hawajakwambia huwa kinabebwa na upepo wakati wa mvua, kinapotea direction. Wananchi mle wamejaa, watoto wadogo, wakina mama, magari, kinapotea direction, kinakaa ndani ya maji zaidi ya lisaa lizima mvua inanyesha, mvua ya kwao, jua linawaka la kwao mpaka hali ya hewa itakapotengemaa ndiyo wanarudi kutafuta njia ya kwenda kugoha (kuegesha) sehemu moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuombe badala ya kusubiri mpaka yowe lilie, tupate maafa kwenye maeneo yale. Kile kivuko amacho tulikichukua zaidi ya miezi sita sasa kimekwenda kutengenezwa kirudi kwenda kutoa huduma eneo ile. Lakini kivuko hicho kikija kije tayari kikiwa kina kivuli kwa sababu kile cha mwanzo kilichokuwepo mvua ilikuwa ni ya kwao, jua lilikuwa ni la kwao. Wakati wa mvua wale wananchi masikini ya Mungu wanavuka huku wameshika roho zao. Ukiwaona wewe mwenyewe Mheshimiwa Waziri huwezi kuamini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nikuombe tusiwe tunasubiri mpaka matukio yanatokea tukirudi tunapeana pole. Hili ninalokwambia ni kama tahadhari, ninaiona kabisa kwa mazingira yale ya namna watu wanavovuka kwa shida eneo lile hebu ichukulie serious. Nimesema zaidi ya watu 50,000 wanategemea huduma kuja Musoma Mjini na wanategemea kuvuka na kivuko hiki. Wakinamama wajawazito wakati mwingine masikini ya Mungu ili waweze kuvuka complication ya kituo cha afya wanatakiwa waje Hospitali ya Mkao Musoma Mjini, wanatumia kivuko hiki, lakini hakiko stable. Nikuombe sana Mheshimiwa Waziri ili ulione hili kwa jimbo lingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la tatu nataka nichangie kuhusiana na bandari. Mheshimiwa Juliana amezungumza vizuri sana bandari ya Musoma. Tunayo bandari pale Wilaya ya Rorya, bandari ya Sota ni bandari ambayo kipindi cha nyuma ikisaidiana na bandari ya Musoma ilikuwa inakuza sana shughuli za kiuchumi kwa watu kutokea Kenya kupitia pale bandari ya Sota kuja mpaka Musoma. Leo bandari zote hizi hazifanyi kazi Mheshimiwa Waziri na bahati mbaya sana bandari ya Sota niliuliza hapa mkasema kwamba kuna fedha mtaingiza kwenye mchakato angalau iweze kufanyiwa marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona kwenye bajeti humo haimo, bandari ya Musoma Mjini haimo. Zile bandari ndiyo ukuaji na ukuzaji wa uchumi wa Mkoa wa Mara. Leo sisi tunafanya shughuli ya uvuvi hatuna watu wa nje kuja kununua Samaki, badala yake wavuvi wanatoa samaki Musoma kupeleka Kenya kitu ambacho ni hatari sana kwa maisha yao. Tunataka mtuambie ili ukuaji wa uchumi wa Mkoa na Wilaya ya Rorya nini mnafanya katika ukuzaji wa hizi bandari ili Mkoa wa Mara uweze ku-stimulate. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wafanyabiashara wengi leo Mheshimiwa Waziri wanakimbia kutoka Musoma wanahamia Mwanza. Wavuvi waliokuwa wanafanya shughuli za kiuvuvi ambao walikuwa wanategemea wanunuzi kutoka Kenya, Uganda hawapo tena ni kwa sababu ya hizi bandari zimekufa.

Nikuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu sijaziona humu ndani, niombe utakapokuja kusimama useme ni nini mpango mkakati wa hizi bandari kwenye maeneo ya Mkoa mzima wa Mara, bandari ya Mkoa wa Mara ya pale Musoma Mjini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini utuambie nini mkakati mlionao wa Bandari ya Sota ambao iko mpakani mwa Kenya, Uganda na Tanzania. Hayo ndio mambo tunayotaka tuyaone sisi kwenye bajeti yako, lazima fedha iende kwenye maeneo ambayo yanakuza, fedha inajirudia yanakuza uchumi wa eneo husika, hutakuwa unaangaika badala ya kupeleka barabara ambayo hayana uchumi inakwenda inafika mwisho inagota imekwishia hapo, sisi tunakuambia peleka barabara maeneo ambayo wale wananchi wa maeneo yale ukuaji wa uchumi utakuwa Wakenya watakuja wengi watapitia pale badala ya kuzunguka maeneo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waganda wale wanaohangika kupitia majini watapitia pale, yaone haya Mheshimiwa Waziri kama vipaumbele vyako kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe mimi nitasema kwamba nitaunga mkono bajeti baada ya haya yote niliyoyazungumza Mheshimiwa Waziri nitakapopata majibu sahihi kuhusiana na barabara ya Mika - Utegi, kuhusiana na bandari zile, kuhusiana na hiki kivuko ambacho kila siku ninavyoongea na wewe juzi mwananchi ananipigia Mheshimiwa Mbunge kivuko kimepotea njia, tuna saa nzima tumekaa kwenye maji tumeshika roho zetu, hatujui mvua iishe muda gani tuendelee na safari, halafu leo niangalie humu nione hakuna fedha iliyotengwa, kivuko mnasema kiko matengenezo yale asilimia 73 kinakamilika lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima nipate haya majibu ili wananchi wajue nusra zake, kama nilivyosema tusisubiri majanga ili uniambie Mheshimiwa Mbunge pole kwa yaliyotokea wakati tuna uwezo wa kuchukuwa tahadhari mapema kunusuru wale wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami nimepata ridhaa ya kuchangia Wizara hii ya Uvuvi na Mifugo, kwa hiyo, nianze tu kwa kumshukuru Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji mzuri na namna ambavyo wamejipanga kuhakikisha yale ambayo wamekusudia kwa maslahi mapana ya wananchi yanatimia. Mwenyezi Mungu awape nguvu ili mwendelee kuitumikia Wizara hiyo vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina mambo mawili kabla sijaanza kuchangia. Kwanza nakushukuru Mheshimiwa Waziri kwa kunipa majosho saba kwenye kata saba kwenye bajeti ya mwaka uliopita; Bukwe, Kigunga, Kinyenche, Nyamagaro, Kitembe, Nyahongo na Mirare. Pamoja na kunipa majosho haya niseme tu Mheshimiwa Waziri, hitaji langu lilikuwa ni zaidi ya hii, kwa sababu shughuli kubwa ya kiuchumi ndani ya Wilaya yangu ukiacha kilimo, shughuli ya pili ni uvuvi, na ya tatu ni mifugo. Kwa hiyo, natamani sana Kata zifuatazo: Kata ya Baraki, Kinyenche, Komugarabo, Nyaburongo, Ikoma, Kisumwa, Kirogoloche na Nyaburongo ziingizwe kwenye Mpango. Nitakuandikia vizuri ili angalau tuone namna gani unatusaidia kwa mwaka wa bajeti unaokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kunipatia fedha hizi za majosho, Mheshimiwa Waziri nikwambie kwamba mpaka sasa hazijaanza kufanya kazi. Sina imani kama wataalam wanakwambia. Hazijaanza kufanya kazi kule vijijini kwa sababu ya namna mlivyozitengenezea utaratibu wa utekelezaji wake. Haya ndiyo tulikuwa tukisema hapa kwamba fedha mnapeleka vizuri, lakini utekelezaji wake unakuwa mgumu sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, mmewaambia Halmashauri itafute Mkandarasi. Inampata Mkandarasi, josho moja mmetenga Shilingi milioni 18; Mkandarasi anatakiwa afanye kwa kiwango kidogo kidogo, ana-rise certificate, Halmashauri inaleta kwenu Wizara, Wizara mnaanza kuandaa malipo, na mpaka uende kumlipa Mkandarasi imechukua muda mrefu. Wamegoma kutekeleza hili. Kwa hiyo, naomba ule utaratibu ubadilike. Pelekeni fedha kwenye Halmashauri kama ambavyo Wizara ya Afya na Wizara nyingine zinavyopeleka fedha, zipelekeni kule. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuwezi kuogopa kupeleka shilingi milioni 18 na wakati Wizara nyingine zinawapelekea mpaka shilingi milioni 500. Unashindwaje kumwamini Mkurugenzi kwa shilingi milioni 18 peke yake? Niliona wakala umeandikwa na Katibu Mkuu, naomba huu muu-review. Wapelekeeni wao wapange namna ya ujenzi wa haya majosho. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, mmepeleka program ya hereni, kuvalisha hereni kwenye masikio ya ng’ombe, sina shida na utekelezaji wake, lakini bei mliyoweka kwa mwananchi wa kawaida shilingi 1,750 ni kubwa sana. Naomba sana muu-review hii ili angalau wananchi wote waweze kupata.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ambalo ni muhimu sana, Mheshimiwa Waziri nimekuwa nikisema, mpaka wa Kirongwe ambao unatuunganisha kati ya Kenya na Tanzania, zaidi ya kilomita 60 ndani ya mpaka ule, kwa maana ukitoka Bukura kule, Roche, unakwenda mpaka Tarime Vijijini, lile eneo liko wazi. Ukimuuliza leo Afisa Mifugo, mpigie simu, atakwambia kwa siku moja ng’ombe wanaopita bila kulipa ushuru siyo chini ya 300 mpaka 500. Wanapita, wanavuka wanakwenda. Hakuna mnada wowote na hakuna Afisa Mifugo yoyote anayesimama, na hata akisimama, eneo la kilomita zaidi ya 60, anasimama wapi ambapo anaweza kutengeneza control?

Mheshimiwa Naibu Spika, tukaleta ushauri hapa kwamba eneo kubwa kama hili muweze mnada wa pili ili angalau mnada ule uweze ku-regulate na kusimamia mapato yenu mnayopoteza.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa napiga hesabu hapa, kwa mwaka fedha mnayopoteza kama wanapita ng’ombe 300, ushuru mliotakiwa mpate shilingi 25,000 kwa ng’ombe, maana yake kwa mwaka mzima ninyi Wizara mmekubali na mmeridhia kupoteza zaidi ya Shilingi bilioni mbili na kitu kwa kila mwaka ambayo ni fedha mngeweza kuikusanya kwa kujenga soko la shilingi milioni 200 au shilingi milioni 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba sana Mheshimiwa Waziri hii aichukulie very serious. Mnaweza mkawa mnakuja mnasema Serikali haina fedha, lakini pale fedha inapotea hadharani. Naomba sana hili, nje ya kujenga soko, muende mka-review bei ya ng’ombe hiyo mnayofanya shilingi 25,000 kwa mfugo mmoja. Wale wananchi wanalalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ujue ukitaka kuchukua fedha, tengeneza friendship. Tengeneza mahusiano kati yako na yule unayechukua kwake. Shilingi 25,000 kwa mfugo ni kubwa. Mtu ana ng’ombe zaidi ya 500 au 600, atatafuta mbinu tu za kuwakwepa ili msichukue ile fedha. Kaeni nao muone namna ya kuzungumza kutengeneza friendship ili waweze kulipa hii kodi ya Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo, niende sasa kuchangia kwenye Wizara ya Uvuvi. Niseme tu kabisa Mheshimiwa Waziri, kiukweli tunashindwa namna ya kukukamata wewe, na kwa sababu Waziri wa Fedha yupo, tumegundua namna ambavyo hatujawa serious sana kwenye sekta ya uvuvi. Hii ndiyo inatu-cost leo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kenya ambayo asilimia ndogo sana ya maji ya Ziwa Victoria ina asilimia tano mpaka asilimia sita imeingia kwao, lakini wao wana-export sangara wengi kuliko sisi Tanzania. Rorya peke yake, mzunguko wa maji ndani ya wilaya, nimezungukwa na maji zaidi ya asilimia 76. Yaani Kenya wana asilimia tano, lakini wana-export sangara wengi kuliko mimi niliyezungukwa na maji kwa asilimia 76. Hatujawahi kujiuliza ni kwa nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, Uganda wale nao leo Mheshimiwa Mbunge alikuwa anachangia hapa asubuhi, wao wameamua, wako serious kwenye uvuvi, wameona namna ambavyo samaki wanavyoendelea kukosekana, wameanzisha uvuvi wa vizimba. Sisi kama Serikali hatujaamua namna gani tunaondoka hapo, hata nikiwauliza, toka tumeanza program ya uvuvi haramu 2015/2016 ni nini tume-archive? Kwa sababu lengo lilikuwa ni kuwanusuru sangara wasiendelee kwisha ziwani. Mbona sangara hawaongezeki badala yake wanapungua? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali, Mheshimiwa Waziri umefanya presentation lakini hujatuambia sasa nini kinachosababisha sangara hawaongezeki, pamoja na kudhibiti na kuwa wakali kwenye uvuvi haramu? Ni kwa nini? Ni kwa sababu hatujaamua kuwa serious. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo wavuvi wangu ndani ya Wilaya yangu ya Rorya, Mheshimiwa Waziri nimekuwa nikikwambia sana; nje ya u-seriousness wale masikini wa Mungu, wanapanda ziwani, wanakaa zaidi ya siku nne au siku tano anatafuta samaki. Anakuwa ameingia gharama zote kuwapeleka wale wavuvi, kununua mashine, chakula na kitu vingine. Akimaliza uvuvi, anashuka chini anakamatwa na watu wanaitwa mama yao. Sijui kama Mheshimiwa Waziri unaifahamu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna watu wanaitwa mama yao, hawana utofauti na wale panya road wa Dar es Salaam. Wanawapiga, wanawanyang’anya hizi mali zao, wanawanyang’anya samaki, wavuvi wanarudi bila kitu, wanalia. Kuna watu Mheshimiwa Waziri wamefilisika; kuna watu kule wametumia mikopo yao kwa ajili ya ku-invest kwenye uvuvi, hawaeleweki; kuna watu wamehama. Leo ukienda Sota pale Shirati, mitumbwi ilikuwa zaidi ya 200 mpaka 300, wamekimbia, kuna mitumbwi 20 tu. Nafiriki Mheshimiwa Naibu Waziri analifahamu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kwenye hili, Mheshimiwa Waziri wa Mifugo, Waziri wa Ulinzi, Waziri wa Mambo ya Ndani na wote ambao wanahusika katika pandikizi hili, mwingilie kati muone namna ya kuwasaidia wavuvi wetu. Wenzetu, ukienda Kenya na Uganda kila leo kule ziwani wanalinda. Wako serious wanalinda rasilimali. Hawa ndiyo ukiwauliza wale wavuvi, utasikia tumepigwa na Waganda, tumepigwa na Wakenya, wanataja hadharani, lakini hatujaona u-seriousness wa Serikali kuwasaidia wale wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kama tunasema tuko serious kusaidia sekta ya uvuvi, tunaisaidiaje? Kama watu wanafilisiwa, kama watu wanaondoka, wakija huku wanakamatwa na kanuni za uvuvi haramu, hatuwezi kuwasaidia. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri kwenye hili atafute namna ambayo tunaweza tukawasilikiza wale wavuvi na namna ya kuwasaidia wale wavuvi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu kwenye hilo, tunazungumza kwamba tuko tayari kuboresha na kuimarisha ulinzi kule ziwani; mtakubaliana nami kwamba katika mali ambayo hailindwi ni samaki. Leo ukienda kwenye madini, tumeweka walinzi kule wanalinda; ukienda pale Tanzanite inalindwa day and night; ukienda kwenye sekta nyingine zozote zile ambazo zinazalisha maliasili zinalindwa; ukienda TANAPA, wanalinda. Leo ninyi ni mashahidi, ukienda ziwani hakuna ulinzi wowote unaolinda malighafi tunazozalisha ziwani ili zisisafirishwe kwa njia haramu kwenda nje ya nchi, hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri, anasema operation zilifanyika mara tatu. Wenzetu kule Kenya na Uganda brother, hawafanyi operation, wako ziwani wamepiga kambi, wanahakikisha wanachokichuma kinarudi ndani ya nchi yao, wanakizalisha, wanakipeleka nje. Sisi tunafanya operation mara tatu, na operation nyingi mnazozifanya ni za kushughulika na hawa wavuvi haramu peke yake. Hamshughuliki na malighafi ambayo inatolewa, wenzetu wanakuja wanachukua ndani ya Tanzania wanapeleka nje, hakuna ulinzi kule ndani, hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa namba, lazima tubuni, tutafute namna ambayo itaimarisha ulinzi kwenye malighafi zetu tunazozalisha ndani ya nchi. Tudhibiti wale ambao wanakuja kwetu wanachukua samaki wanapeleka nje. Mtawapa wengine sifa ya kuonekana wana-export zaidi kwenda nje ya nchi kuliko sisi. Leo tunazungumza, Kanda ya Ziwa, zaidi ya asilimia 75 ya product earning ambayo tunaipata kama mapato ya nje, inatoka Kanda ya Ziwa, lakini wale ndio kila siku mnasikia wanalia, wanapigwa, wananyang’anywa mali zao, hawana vitendea kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi vizimba tunavyozungumza, vinazungumzwa kwenye karatasi, kule ukienda vizimba halisia hakuna. Namna gani tunawasaidia wale wananchi wa Kanda ya Ziwa? Mkoa wa Mara, nje ya kilimo shughuli kubwa ya kiuchumi kwenye Mkoa ule ni uvuvi. Sisi tunatamani tuone namna gani Wizara mmejipanga kusaidia kwenye sekta ya uvuvi Mkoa ule wa Mara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, kwenye hivi vizimba ambavyo tunapitisha kwenye bajeti yake leo, ahakikishe angalau asilimia 60 mpaka 70 inakwenda kule kuwasaidia wananchi wetu, kwa sababu vinginevyo tutaendelea kutegemea uvuvi wa baharini, uvuvi wa kwenye maziwa lakini hauko productive. Kule wanakokwenda masikini ya Mungu mnajua namna ambavyo wanakutana na zile changamoto. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri aone namna ya kuwasaidia hawa. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Jafari. Kengele ya pili hiyo.

MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili nami niweze kuchangia Wizara hii ya Ardhi. Nianze tu kwanza kwa kuungana na wenzangu ambao tangu asubuhi wameshiriki kwa pamoja kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa tuzo na zawadi ambazo wenzetu wameweza kumuona na kumtunuku. Kubwa mimi niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa namna ambavyo kwenye kila sekta ameweza kuweka mkono wake ili kusaidia, lakini lengo likiwa ni moja tu, kuwasaidia wananchi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye Wizara hii tu peke yake Mheshimiwa Rais ametoa zaidi ya bilioni 50 kwa ajili ya kuhakikisha angalau ardhi ya nchi hii inapangwa, kupimwa pamoja na kumilikishwa. Haijawahi kutokea kwenye ziada ya bajeti kutoa fedha nyingi kiasi hicho ka bajeti ya mwaka jana ambayo angalau imetumika kuanza kupanga, kupima na kumilikisha kwenye baadhi ya maeneo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana fedha ikawa ni ndogo na tukawa hatuoni impact yake, lakini haya yote hatuwezi kuyaona ni kwa sababu ya ukubwa wa eneo la ardhi hii ambalo halijawahi kupangwa, kupimwa na kumilikishwa. Tunazungumza zaidi ya asilimia 75 ya nchi hii haijawahi kupangwa, kupimwa na kumilikishwa. Asilimia 25 pekee ndiyo iliyopangwa, kupimwa na kumilikishwa. Na zaidi ya asilimia 60 ya nchi hii haijapangwa. Kwa hiyo unaweza ukaona kwamba yawezekana fedha imetoka, Wizara ikaichukua ikafanya kazi lakini impact yake isionekane kwa haraka kwa sababu ya maeneo mengi bado hayajafanyiwa kazi ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi leo nitajikita sana kwenye kutoa ushauri. Ninajua mchango mkubwa na kazi kubwa wanayoifanya Mawaziri hawa. Kwa sababu kama wenzangu walivyochangia, migogoro ya ardhi ni mtambuka. Hapa leo tukipanga na kupima maeneo yote nchi hii bado tukubaliane kwamba kuna baadhi ya maeneo kutakuwa na migogoro ya ardhi, haiwezi kwisha yote kwa pamoja. Tunachojitahidi sisi ni kuhakikisha ile migogoro ambayo tunaishauri Serikali, ni kuhakikisha angalau inapungua kwa kadiri inavyowezekana ili angalau kutoa haya ambayo yangekuwa yakichangiwa humu ndani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nitajikita kwenye sera katika ushauri wangu. La kwanza ninaloliona hapa ambalo linaleta shida kubwa humu ni Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995. Mimi nichukue nafasi hii kumuomba sana Mheshimiwa Waziri, haya yanayozungumzwa, kitu pekee ambacho kinaweza kikamuokoa ni kuharakisha ile Sera ya Taifa ya Ardhi ambayo imeshapitwa na wakati. Sera ya Taifa ya Ardhi ndiyo ilizaa mabaraza ya ardhi. Mabaraza ya ardhi ngazi za vijiji, kata na wilaya yote haya kuna confusion ya sheria namna ya uratibu wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kukiwa kuna mgogoro kwenye kijiji umetatuliwa na baraza la ardhi la kijiji na haujakwenda sawa sawa atalaumiwa Waziri husika; pamoja na kwamba na yale mabaraza hayawajibiki kwa Mheshimiwa Waziri moja kwa moja ilhali yametajwa kwenye sheria kwamba yanawajibika chini ya mkurugenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa mimi niombe, sera ambayo itatupelekea mabadiliko ya sheria itaondoa hii changamoto iliyopo. Mimi niombe sana kwenye hili, Mheshimiwa Waziri wa Ardhi na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI mkimbizane na Mheshimiwa Waziri wa Fedha ili tuone namna tunavyoweza kufanya review kwenye sera ili hatimaye tupate sheria nzuri. Haya mabaraza ya ardhi yote yasiwe na confusion. Baraza la ardhi la wilaya wanawajibika kwa Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, mabaraza ya ardhi ya kata na vijiji yanawajibika kwa Waziri wa TAMISEMI. Hii confusion haiwezi kuwa sawa sawa. Kwa hiyo unakuta tayari huku wameharibu, ikija kufika kwenye baraza la ardhi ngazi ya wilaya, hata kama Waziri ataonekana ametatua bado inarudi kwenye Wizara ile ile ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe, ili kuondoa hii confusion, kwa sababu imetajwa kwenye sheria, ni lazima tukimbizane kutengeneza sera uya ardhi na kupata sheria ambayo ita-regulate na itasimamiwa kwa pamoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, tukubaliane; sehemu mbili ambazo zinaweza zikashughulika na changamoto ya migogoro ya ardhi ni mabaraza ya ardhi pamoja na Tume ya Taifa ya Mipango. Tume ya Taifa ya Mipango, tutakubaliana hapa; kwa mwaka wa jana na mwaka huu peke yake imetengewa bilioni 1.5. kuandaa mpango wa matumizi bora ya kijiji kimoja yanagharimu zaidi ya milioni 11 mpaka milioni 15, kijiji kimoja. Leo mnawapa 1.5, maana yake nini; atakwenda kuandaa mpango wa matumizi bora ukigawanya pale ni vijiji 100 tu peke yake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake ni kwamba, Mpango wa Tatu wa Taifa wa Maendeleo hautakidhi na mpango huu ambao tunazungumza hapa, ambao Mheshimiwa Waziri wa Fedha umeuwasilisha. Wakati huo huo unakuwa kinyume na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ilani ya Chama cha Mapinduzi hapa inasema, angalau kwa mwaka vijiji vinavyotakiwa kupangiwa matumizi yake visipungue 750. Maana yake ni kwamba, kwa miaka mitano, wame-project mpaka mwaka 2025 tuwe tuna vijiji elfu tatu, mia sab ana kidogo. Lakini sasa hawa watu mnawapa bilioni 1.5, kwa mwaka anapanga vijiji 100 peke yake. Maana yake ni kwamba anakwenda kinyume na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi na Mpango wa Tatu wa Mandeleo ya Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha, tutafute namna ya kuinusuru hii Wizara. Ile Tume ya Taifa ya Mpango haya yote yanayozungumzwa inatakiwa iende site, ishughulike na kutatua migogoro iliyopo kati ya wafugaji na wakulima na migogoro ya mipaka iliyopo. Sasa haiwezi ikatatua kama haina fedha ya kufika kwenye maeneo husika. Hii ndiyo instrument ambayo inatakiwa iende ikashughulike na migogoro hiyo, haina fedha, wanakwendaje? Wanatatuaje migogoro?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi niombe, solution ya kwanza kabisa ni kuongezewa fedha. Tuwape fedha angalau waendane na Ilani ya Chama Cha Mapinduzi inavyosema pamoja na Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa. Vinginevyo tutafanya 25 hawatakuwa na fedha ya kufanya hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshauri Mheshimiwa Waziri wa Fedha, fedha ipo. Mheshimiwa Mdee alizungumza asubuhi hapa vizuri sana, fedha ipo na sehemu ambayo ipo, ukisikiliza Hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa nane, anasema, hakufikia malengo ya makusanyo ya kodi ya ardhi kwa sababu kuna Mashirika ya Umma hayalipi kodi. Wanadaiwa zaidi ya asilimia 70; na wanazalisha zaidi ya Shilingi bilioni 78 Mashirika ya Umma zaidi ya 114. Maana yake ni nini? Yale Mashirikia yakibanwa yakalipa ile Shilingi bilioni 78, tutapata Shilingi bilioni 10 iliyokuwa inaombwa na Tume ya Taifa ya Mipango kwenda kutekeleza jukumu hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu haya ni Mashirika ya Umma, ni Mashirika ya Serikali, yanaingia kwenye Bajeti kila mwaka, yatenga fedha kwa ajili ya kulipa kodi ya ardhi na hayalipi, leo hii jioni naomba, kesho tutakapokuwa tunahitimisha, Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Waziri Mkuu angekuwepo tungemwomba, watoe maelekezo na matamko ya haya Mashiriki ili yaweze kubanwa kulipa hii fedha. Kwa sababu vingenevyo, Wizara ya Ardhi kila mwaka inapanga bajeti na ikipanga bajeti inaonesha kwamba Mashirika yaliyopo yanatakiwa kulipa kiasi gani cha kodi ya ardhi, halafu unafika mwishoni, hayalipi ile fedha, unakwenda mwaka mwingine. Hawa watu mtawakamua kadri mnavyoweza lakini hawatafika lengo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa haya ni Mashirika ya Umma, kwa nini mwananchi mnyonge tunamwambia lipa kodi ya ardhi? Shirika la Umma ambalo linatengwa kwenye bajeti, linapewa fedha ya Serikali, hawalipi. Namwomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha, kigezo kimojawapo cha Mkurugenzi yeyote wa Shirika la Umma ambaye halipi kodi ya ardhi ili angalau ile fedha iende kushughulikia kutatua migogoro ya wananchi, iende ikatumike kwa shughuli nyingine; na iwe ni kipimo kimojawapo cha kumtathmini kama kweli anaweza kufanya kazi ile. Kwa sababu haina maana kama mashirika mengine yanalipa fedha, halafu wengine hawalipi. Mashirika 114 nchi hii hawalipi, na tunakwenda kumaliza mwezi wa Sita hawatalipa. Wanabeba madeni, yanakwenda mwaka ujao, hawatalipa. Lini Wizara hii itafikia lengo? Lini itapata fedha ili iende kuweza kupanga na kupima maeneo ambayo hayajapimwa? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwamba ili tuweze kumnusuru Mheshimiwa Waziri na hii Wizara ya Ardhi, tuhakikishe angalau wale ambao wanatakiwa kulipa kodi kwa wakati, walipe kwa wakati na kwa mujibu wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, sambamba na hili kwa Mheshimiwa Waziri, nilisema leo sitakuwa na la kulalamikia, nilitaka tu nishauri kwa namna ambavyo imekaa. Namwomba Mheshimiwa Waziri, tuliwahi kuzungumza toka mwaka 2021 kuhusiana na Housing Policy, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Mheshimiwa Mchechu kurudi kwenye Shirika la Nyumba la Taifa. Najua kwa namna anavyofanya kazi vizuri, ataanza kazi muda wowote wa ujenzi wa hizi nyumba. Shida yangu ni kwamba, anapooanza shughuli zile za ujenzi, kelele huwa zinakuwa nyingi kwamba bei za nyumba zinakuwa kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuwa nikisema sana, bei ya nyumba inaweza kuwa regulated na Housing Policy, lakini inaweza kuwa regulated kama tutaipitia tukaainisha maeneo yote namna ya ku-regulate. Namwomba sana Mheshimiwa Waziri pamoja na watu wake wote ndani ya Wizara; Mheshimiwa Naibu mimi naamini kwamba wewe ni kijana umeingia na unafanya kazi vizuri, tuchangamkie hii ili yule atakapoanza Shirika la Nyumba kukimbizana na ujenzi wa nyumba za gharama nafuu, mwananchi aweze kupata nyumba kwa gharama nafuu kadri inavyowezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba maeneo ya mpakani, ya maziwani na baharini tuone namna ya kuweka maboya, tuone namna ku-identify, kutenganisha mipaka kati ya Tanzania na zile nchi mbili ili angalau tuondokane na yale ambayo yanayotokea kule. Wananchi kule wanavamiwa, wanapigwa na maeneo mengine wanaumizwa. Naomba sana, mipaka ile, yale maboya yakiwekwa yatasaidia sana maeneo ya maziwa na baharini ili angalau mvuvi wa Uganda anapokuja akiona yale, ajue nikienda naenda Tanzania, huku ninapokwenda naenda kuchukua cha watu. Watanzania nao vivyo hivyo. Naomba sana, pamoja na maeneo mengine, mwone namna ya kulifanya hili kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi kuweza kutoa mchango wangu kwenye Wizara hizi mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza kabisa, niungane na wenzangu kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kuridhia na kukubali ushauri wa Bunge wa kutenganisha Wizara hizi na hatimaye kutuundia Wizara mpya ya Mipango na Uwekezaji. Kipekee kabisa nichukue nafasi kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuliona hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nimshukuru kwa kutupa mtu ambaye ni sahihi, tukiamini kabisa kwamba lengo na dhumuni la Wabunge tulikuwa tukilizungumza kuhusiana na Mipango kapewa mtu ambaye ni sahihi na sasa imani yetu ni kwamba Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo atatuvusha kwenye hili. Akiamini kabisa kwamba Wizara hii ya Mipango na Uwekezaji inapaswa kuwa ndiyo dira, mwelekeo na catalyst ya kutuonesha wapi tunatakiwa kwenda kama nchi na isiwe mipango ya mwaka mmoja peke yake naamini kwamba itakuwa ni mipango endelevu ya miaka nenda rudi, yote hiyo ni kutuonesha kwamba kama Taifa tunapaswa kuelekea wapi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu yangu Mheshimiwa Prof. Kitila Mkumbo, wewe ni msomi nafikiri kwa sababu wewe ni Professor, unajua, hakuna mipango mizuri ambayo inaweza ikafanyika, kwa uchache tu kwanza, bila kuzingatia research. Pili, bila kuoanisha na kutazama sera (policy) mbalimbali zinazoshabihiana kwenye Wizara na Sekta husika, hili ndilo inawezekana ikawa ufaulu mkubwa sana wa Wizara hii kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, mchango wangu utajikita hapa. Kwanza, ambalo ningetamani nikushauri ni kwamba pamoja na kwamba unaweza ukawa na mipango mizuri uliyotuwasilishia leo hapa lakini mipango yako ningekushauri Mheshimiwa Waziri iende ikatazame sera mbalimbali za kisekta hasa sekta za uzalishaji, ambazo kimsingi zitashabihiana na kuku-boost kwenye Mpango wa Taifa 2023/2024.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sera mbalimbali ambazo zimepitwa na wakati haziwezi kusaidia Mpango wa Taifa linalokusudia kwenda miaka mitato, kumi kwenda mbele. Mfano, kuna Sera ya Taifa ya Ardhi ya Mwaka 1995, sera hii kwa namna ambavyo ameizungumza Mheshimiwa Waziri, kwenye wasilisho lake sera hii inagusa maeneo mengi. Migogoro inayozungumzwa na Waheshimiwa Wabunge, ambayo iko TANAPA, TAMISEMI na Wizara ya Ardhi inagusa wananchi wanyonge ambao ni wananchi maskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna yoyote kama Taifa likiwa lina mipango mizuri inayogusa wananchi maskini bila kutazama namna ya kutatua ile migogoro hatuwezi kupata ile furaha tunayoitamani kutoka kwa wananchi wetu tunaowawakilisha. Kwa hiyo, ningetamani sana Mheshimiwa Waziri, kama nilivyosema kwa sababu Wizara yako ni catalyst iende ikatazame namna ya kufanya maboresho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hauwezi kwenda na mipango ya miaka mitano mbele tunakwenda kuzungumzia 2030, huku una sera ya mwaka 1995 yaani miaka 18 iliyopita kwa population ambayo ilikuwa haifiki milioni 20 tuitumie kupanga mipango ya nchi ya kwenda zaidi ya mika 10 mbele. Kwa hiyo, ningetamani Mheshimiwa Waziri, uende ukakae na utoe ushauri kabisa kwenye Wizara za Kisekta hizi ambazo kimsingi ndizo zinapaswa zikusaidie wewe kuhakikisha mipango inakwenda kwenye Wizara hii, wafanye maboresho ya sera ambazo zimepitwa na wakati, ikiwemo na hii Sera ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo, Mheshimiwa Waziri kwanza utapunguza urasimu kwa maana ya kwamba utaboresha Sekta ya Uwekezaji ambayo iko chini ya Wizara yako. Pili, utakwenda kupunguza migogoro ya miingiliano kati ya Wizara zote tatu ambazo kimsingi ndiyo wananchi wanyonge wanakotoka. Niliwahi kusema hapa GN ya eneo moja inaweza likatolewa na Wizara tatu tofauti, yaani TAMISEMI, inatoa GN ya kuanzisha kijiji, Wizara ya Ardhi inatoa GN ya kutengeneza mipaka lakini vilevile ukienda kwenye upande wa maliasili nao wana GN yao ya maeneo ya hifadhi. Kwa hiyo, kule kunakuwa na kelele nyingi Mheshimiwa Waziri, kwanza kelele za wananchi maskini wanaozungumza haziwekwi, lakini wewe pia Wizara yako kwa maana ya uwekezaji hauwezi kuwa na tija kama maeneo haya yatakuwa hayajafanyiwa kazi. Kwa hiyo nikuombe sana ulione hili namna ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunazungumzia mipango sehemu ya ardhi iliyopimwa ni zaidi ya asilimia 25 peke yake, lakini mipango unayoizungumza inakwenda kupangwa kwenye eneo hilo hilo la ardhi, kwa hiyo, ni lazima uone namna ambayo unaweza kupanga eneo hili likapimwa kwa maana ya nchi nzima ili mipango yako iende sambamba na kuweza kuleta faida.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili Mheshimiwa Waziri ambalo ningekushauri, Bunge lililopita tulipitisha hapa Itifaki ya Huduma za Kibiashara za Nchi za Kusini mwa Afrika, ningeomba uone namna ya Itifaki hii kama Waziri wa Uwekezaji na Waziri na Mipango kutoa elimu kwa wananchi wazawa, wawekezaji wa nchi hii ili waone namna ya kuchangamkia hii fursa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili Mheshimiwa Waziri, ujiandae namna ambavyo Nchi wanachama ambazo zimekubaliana kufanya shughuli za kibiashara kwenye nchi hizi, namna zitakavyowekeza Tanzania na namna wananchi watakavyoweza kunufaika kama Tanzania. Mara nyingi tumekuwa tukipitisha Itifaki hizi lakini tunakosa mtu halisi wa kusimamia na kutafsiri nini ambachoo Bunge limekusudia. Kwa hiyo, ningekuomba Mheshimiwa Waziri, uone namna ya kulifanya hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu Mheshimiwa Waziri, mipango yako yote ningetamani Mipango ya Taifa lazima iendane na Mipango ya Wizara, Mipango ya Taasisi na Mipango ya Halmashauri. Hatuwezi kuwa na Mpango wa Taifa halafu huku chini kwa maana ya Taasisi, Halmashauri nazo zina mpango tofauti na mpango ambao unaendana na wewe. Kwa hiyo, kama Halmashauri zinaandaa mpango maana yake ni lazima zioane na ule Mpango wa Taifa, hatuwezi kuwa na mpango mdogo Halmashauri ambao kwako wewe hausimamii na hauna namna ya kuusimamia, maana yake tutakuwa tuna mipango mingi tu, kwamba huku Taasisi zina mipango yao lakini sisi tuna mpango mkubwa wa Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho Mheshimiwa Waziri, ninaomba kwa kuwa tayari tunakwenda kuinua uchumi ninayo barabara yangu ambayo nimeizungumza sana, siyo barabara yangu ni barabara ya Mkoa wa Mara, kimsingi barabara ile inatuunganisha kati ya Kenya na Tanzania. Barabara ile inapita katika Jimbo langu, nimezungumza leo nilipokuwa nauliza swali nilikuomba Mheshimiwa Waziri, barabara hizi ambazo ni kiungo cha uchumi kati ya nchi na nchi, kati ya Mkoa na Mkoa na Wilaya na Wilaya zipewe kipaumbele katika uwekezaji wa mpango ili angalau tuone namna ambavyo zinaweza kuinua uchumi wa nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi barabara za ndani zipo lakini barabara kubwa zinazounganisha kati ya nchi na nchi, Mheshimiwa Waziri uone namna ambavyo mnaziwekea fedha kwa sababu Mheshimiwa Waziri wa Fedha yuko hapo ziwekewe fedha ili angalau ziweze kuinua uchumi kutoka maeneo jirani na uchumi wa wananchi wote kwa ujumla wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Ahsante naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. JAFARI W. CHEGE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Niungane na wenzangu kwanza kumshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia TAMISEMI, kwa niaba ya wananchi wa Kata ya Goride Kijiji cha Nyamusi kwa kutupatia fedha. Sasa nimepigiwa simu na Injinia wa TARURA Mkoa, kuwa wametupatia fedha zaidi ya shilingi milioni 92 kwa ajili ya ujenzi wa daraja ambalo lilikuwa linaunganisha wananchi wa Kitongoji cha Mariwa na Kijiji cha Nyamusi. Nachukua nafasi hii kuwashukuru sana kwa sababu katika daraja hili wananchi wengi wamekuwa wakipoteza maisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimesimama hapa kwa masikitiko makubwa sana. Kwanza, niseme tu, mimi ni miongoni mwa wale Wabunge ambao hata baada ya Bunge hili kukamilika na kurudi jimboni, sijui ni barabara ipi ambayo inaweza ikanifikisha maeneo ambayo natakiwa kuzungumza na wananchi, kwa sababu barabara zote kati ya 12, barabara nane hazipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Jimbo la Rorya maeneo mengi shughuli kubwa ya kiuchumi tunayoitegemea ni ziwa. Katika barabara 12, barabara nane zinatupeleka maeneo ambayo halmashauri ndiyo inategemea kukusanya mapato, ambayo ni maeneo ya ziwani. Katika barabara 12, barabara nane zote hazipitiki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikumbushe kidogo, tarahe 31 mwezi wa Kwanza, ilikuwa ni siku ya Jumatano kilikuwa ni Kikao cha Bunge hili, alisimama Waziri wa Fedha na akaahidi ndani ya Bunge hili baada ya baadhi ya Wabunge kuuliza maswali ya nyongeza na maswali ya msingi. Akasema atahakikisha fedha ya dharura ya utengenezaji wa barabara inakwenda kwenye majimbo ambayo, kwenye maeneo yote ya halmashauri ndani ya nchi hii, ambako barabara hazipitiki. Akaendelea mwishoni akasema, atahakikisha fedha hizi zinakwenda kabla ya Bunge hili kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo ni siku ya Jumanne, tuna siku mbili zimesalia hakuna fedha yoyote ya dharura iliyokwenda kushughulika na barabara hizi. Wananchi wanateseka, hakuna namna ambayo unaweza ukafika kutoka eneo moja kwenda maeneo mengine. Kwenye halmashauri zetu sisi tunategemea shughuli za kiuchumi magari yaende yakafanye ulanguzi kwenye maeneo ya ziwani, kwa ajili ya kuchukua samaki kwa wavuvi. Magari hayafiki. Mimi ni Mbunge ambaye nimeenda kwenye maeneo hayo, nakwama zaidi ya mara mbili, nasukumwa na wananchi. Una majibu gani ya kuwaambia hawa wananchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nasema, kwa kuwa hoja ya leo tunaizungumza hapa na tunachangia, Mawaziri watapata nafasi pia ya kuchangia na siyo kuhitimisha hoja, kwa sababu hoja kwa mujibu wa kanuni zinahitimishwa na Wenyeviti wa Kamati. Naomba kwa ridhaa yako, kwa hizi siku mbili zilizosalia na nitaomba Waheshimiwa Wabunge mniunge mkono, tulete Hoja ya Dharura itakayojadili barabara za dharura nchi nzima kwa umoja wake na tutoe maazimio ya moja kwa moja yatakayokwenda Serikalini kwa ajili ya utekelezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiendelea hivi tunazungumza, Waheshimiwa Mawaziri watasimama hapa kujibu hoja, bado kule wananchi ni shida. Hebu niambie, leo kama kauli imetoka kwa Waziri wa Fedha mwenye dhamana kwamba atahakikisha kuwa fedha inakwenda kabla ya tarehe 31, mimi leo nakwenda Jimboni nawaambia nini wananchi? Kwa sababu wameisikia Serikali na Waziri mwenye dhamana amesema kabla ya Bunge kwisha fedha zitakuwa zimekwenda. Hakuna fedha maeneo yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Waheshimiwa Wabunge waniunge mkono, ndani ya hizi siku mbili kama hakuna fedha ya dharura, tulete hoja ndani ya Bunge hili, tujadili kama tulivyokuwa tukifanya maeneo mengine. Tuliwahi kujadili hapa kuhusiana na issue za kilimo. Kuna maeneo ambayo wakulima walikuwa na changamoto, tukaleta hoja, tukajadili na Serikali ikapeleka fedha. Kwa maelekezo mahususi au azimio ndani ya Bunge, ninaamini hili linaweza likawa suluhisho kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni issue ya Madiwani kusimamia Miradi ya Maendeleo; utakubaliana nami kwamba, hakuna sehemu ambayo haisimamiwi kwa sasa hivi kama miradi ya maendeleo maeneo mengi ninayokwenda nchini. Kwa mfano, kwangu hakuna Diwani anayekwenda kukagua shughuli za kimaendeleo zinazofanyika ndani ya Jimbo. Kwa nini? Kwa sababu hawana fedha, hawana uwezesho wa halmashauri kuwapeleka kukagua yale maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Wizara kwa maana ya TAMISEMI, ipeleke maelekezo mahususi kwamba miradi yote ya maendeleo Madiwani wote wakague kama mnavyofanya ndani ya Bunge. Sisi tunapata nafasi ya kwenda kukagua miradi ya maendeleo, tunakuja kuchangia ndani ya Bunge. Madiwani wasipokwenda kujiridhisha fedha za miradi ya maendeleo maana yake ni nini? Watakuwa wanaletewa makabrasha ndani ya Vikao vya Madiwani bila kujua huo mradi unaendeleaje. Ndiyo maana unaona miradi haikamiliki, upotevu wa fedha unakuwa mwingi na bahati mbaya sana sisi Wabunge wakati vikao vinafanyika tunakuwa hatupo maeneo ya majimboni, wengi tunakuwa huku. Kwa hiyo, naomba Wizara ya TAMISEMI itoe mwongozo mzuri kwenye maeneo haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, natambua umenipa dakika tano, mapitio ya kanuni. Nakubaliana kabisa na Kamati yafanyike mapitio ya Kanuni ili angalau Vikao vya Baraza la Madiwani viweze kufanyika wakati ambao Wabunge tupo Majimboni tuweze kushiriki kutoa michango ya kusimamia miradi hii ya maendeleo.