Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Answers to supplementary Questions by Hon. Khamis Hamza Khamis (170 total)

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Wizara ya Mambo ya Ndani, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, tumeshuhudia katika maeneo mengi, Jeshi la Polisi limeshindwa kufika kwa wakati kwenye matukio kwa sababu za kukosa mafuta na matengenezo ya magari. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ustawi wa jamii yetu unategemea sana ulinzi na usalama unaofanywa na Jeshi letu la Polisi. Swali la kwanza, je, Wizara haioni sasa ni wakati muafaka wa kufanya marekebisho hayo ya kisheria?

Mheshimiwa Spika, pili, Wizara haioni ni muda muafaka sasa kupeleka hizo fedha moja kwa moja kwa Wakuu wa Polisi wa Wilaya badala ya kupitisha kwa Wakuu wa Polisi wa Mikoa ambapo imetengeneza urasimu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Husna Sekiboko, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza amesema kwamba hatuoni haja ya kufanya mabadiliko ya sheria hii? Mabadiliko ya sheria siku zote yanakwenda na mahitaji. Inawezekana ikawa kuna hitaji la kufanya hivyo, lakini sheria hii ikawa iko hivi hivi mpaka tufike wakati tuone namna ambavyo tunaweza kufanya mabadiliko ya sheria hii.

Mheshimiwa Spika, nataka kumfahamisha Mheshimiwa Mbunge kwamba ukiangalia Sheria ya Bajeti, kuna kitu kinaitwa vote holder na kuna kitu kinaitwa sub-vote holder. Sasa vote holder moja kwa moja anayo IGP na sub- vote holder anayo RPC. Kwa hiyo, fungu likitoka kwa IGP linakuja kwa RPC. Huo ndiyo utaratibu halafu sasa ndiyo zinagawiwa Wilaya husika kama ambavyo tumeeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama sasa inafika wakati tunahitaji mabadiliko ya sheria hii, basi acha tulichukue hilo tukakae na wadau halafu tuone namna ambavyo tunaweza tukalifanyia mabadiliko. Kwa sababu, suala la kufanya mabadiliko ya sheria is a matter of procedure… (Makofi)

SPIKA: Unajua Waheshimiwa Wabunge huwa mnapiga makofi ambapo hamjui hata mnapiga makofi ya nini? (Kicheko)

Ahsante, malizia kujibu. Umemaliza eeh!

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Ndiyo.
MHE. JACKLINE K. ANDREA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii niweze kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Pamoja na kwamba tunajua Serikali ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli inajitahidi kupunguza ajali za bodaboda, tukiangalia kwa mwaka 2019 tulikuwa na ajali 567 lakini mwaka 2020 tuna 240. Je, Jeshi la Polisi lina mpango gani wa kuhakikisha ajali hizi zinapungua zaidi? Tukiangalia wahanga wakubwa ni vijana na wanawake ndiyo wanaopata shida ya kupoteza vijana ambao ni nguvukazi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; utafiti unaonyesha askari wastaafu wanachelewa kupata mafao yao, je, Wizara husika ina mpango gani wa kuhakikisha askari hawa baada ya kustaafu wanapatiwa mafao yao kwa haraka ili kuepusha wanapokuwa kazini kuchukua rushwa ili kujilimbikizia akiba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika jibu la msingi inaonekana Mheshimiwa tumempa sababu moja au njia moja ambayo tunaweza tukaitumia katika kuepuka hizi ajali. Zipo njia ambazo tumeshazichukua kama Serikali na nyingine tuko mbioni kuzichukua kwa kushirikiana na Wizara nyingine au kushirikiana na taasisi nyingine kuhakikisha kwamba hizi ajali za barabarani zinapungua. Cha kwanza tumefikiria kuendelea kuwafundisha zaidi hasa vijana wa bodaboda namna ya kutumia alama za barabarani ambazo zina uwezo mzuri wa kuwaeleza kwamba wanakoelekea wanaweza wakapata ajali.

Mheshimiwa Spika, lingine tuna mpango sasa wa kutengeneza mfumo wa kufunga au ku-control ajali kwa kutumia vidhibiti mwendo, ambapo tunahisi hivi vinaweza kupunguza ajali. Pia tuna mpango wa kufanya marekebisho ya sheria ambayo yanakwenda moja kwa moja kwenye masuala ya faini na adhabu katika mambo haya ya usalama barabarani.

Mheshimiwa Spika, aidha, napenda nichukue fursa hii kumwomba Mheshimiwa Mbunge atusaidie pia kuwaelimisha vijana kwa sababu naamini katika mkoa wake vijana wa bodaboda wapo, basi azidi kuwaelimisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda pia kujibu swali la pili la Mheshimiwa Mbunge kuhusu mafao ya Askari. Kwa kweli Wizara inajitahidi sana kuhakikisha kwamba tunawalipa wastaafu posho zao mara tu baada ya wao kustaafu. Katika kipindi cha 2018/2019 tumejitahidi kati ya wastaafu 591; jumla ya wastaafu 479 tayari tulishawapatia mafao yao na sasa hivi wengi wanaishi maisha mazuri.

Mheshimiwa Spika, kikubwa kinachokuwa kinatukabili kama sehemu ya changamoto, inafika wakati inakuwa OC nazo na bajeti nayo inakuwa mtihani, kwa hiyo, ndiyo maana kuna wakati wanachelewa kidogo kulipwa. Hata hivyo, namwomba Mheshimiwa Mbunge, kama itakuwa kuna mtu ambaye hajapata mafao yake na amestaafu, basi tukitoka hapa tuonane, tuone tunamsaidia vipi.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. SALOME W. MAKAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi nami niulize swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, lipo tatizo la msingi la ajali za barabarani kwa bodaboda na vyombo vingine vya usafiri. Tatizo hili ni Kitengo cha Usalama Barabarani kugeuza kitengo hiki kama chanzo cha mapato. Watu wanakwepa matrafiki, wanakimbia kwa sababu ukikamatwa hakuna onyo, ni faini. Bodaboda siku hizi wanakamatwa kwa kukimbizana na trafiki. Nadhani hii inasababishwa na uzee wa sheria hii ni ya mwaka 1973. Ni lini Serikali italeta mabadiliko ya Sheria ya Usalama Barabarani ili tufungue mjadala wa namna gani tutaiboresha ili kupunguza ajali za barabarani? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDAIN YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Salome, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nimtoe hofu Mheshimiwa Salome, Muswada huu uko njiani, muda wowote tutauleta tuje tuujadili tuone namna ambavyo tunaweza tukafanya mabadiliko ya baadhi ya sheria hizi. Mheshimiwa asiwe na wasiwasi, tuko mbioni kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, siyo kweli kwamba dai la ekari 495 ni jipya, bali ni ahadi ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani mbele ya Mheshimiwa Rais wakati huo alipofanya ziara Mkoa wa Rukwa kwamba watawakabidhi wananchi ekari 495. Lililokuwa linasubiriwa ni kukabidhi kwa maandishi kwa sababu Jeshi la Magereza limekuwa likisema kwamba hatuwezi kufanyia kazi matamko ya wanasiasa mpaka tupewe barua kutoka Wizarani. Ni lini Wizara itawapa barua Jeshi la Magereza ili kukabidhi hizo ekari 495 kwa wananchi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa tamko hili limepelekea Askari Magereza sasa kuingia kwenye mgogoro mkubwa na wananchi na kuwanyanyasa kwa kuwapiga na mara ya mwisho juzi tu hapa nilikuwa huko Jimboni, mama mmoja (na nikikurushia clip utaona) amepigwa na kugaragazwa kwenye matope. Je, Wizara iko tayari kuunda Tume itakayokuja kuchunguza unyanyasaji unaofanywa na hawa Askari Magereza na watakaobainika kunyanyasa wananchi hatua kali za kisheria zichukuliwe iwe fundisho kwa wengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako, naomba kujibu maswali ya Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza tufike wakati tukiri kwamba kuna baadhi ya maeneo bado yana mivutano baina ya wananchi na Kambi za Magereza. Swali kwamba ni lini tutatoa hilo eneo, suala la utoaji wa eneo linahitaji taratibu, siyo suala la kusema tunakwenda na kutoa.

Mheshimiwa Spika, lingine amesema watu wananyanyaswa, wanapigwa, kitu ambacho tunakifanya kupitia Wizara, kwanza tutachunguza, tukiona kwamba kuna Maafisa wetu wa Magereza ambao wanahusika na unyanyasaji huo, hatua kali tutazichukua kupitia Wizara yetu.

Mheshimiwa Spika, ahsante.
MHE. DAIMU IDDI MPAKATE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Jimbo la Tunduru Kusini lina tarafa tatu, Tarafa ya Nalasi, Lukumbule na Sakata na zote zimepakana na Mto Ruvuma, kwa ng’ambo ni Msumbiji, lakini katika Jimbo hilo Kituo cha Polisi kiko kimoja tu kipo kwenye Tarafa ya Nalasi peke yake. Swali la kwanza, je, Serikali haioni ni muhimu sana kwa sasa kukamilisha Kituo cha Polisi Lukumbule ili kiweze kutoa huduma kwa wananchi wa mipakani?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, Lukumbule ni sehemu ambayo watu wengi wanapitia kwenda na kutoka Msumbiji katika harakati za kufanya biashara. Wananchi wa Msumbiji wakija Tanzania hamna mahali popote wanapopita tunawapokea kiurafiki, lakini sisi Watanzania tukienda Msumbiji tunakamatwa wanapigwa, wananyanyaswa na kunyang’anywa mali zao. Je, Serikali haioni sasa ni muhimu kuharakisha mazungumzo ya kuanzisha Kituo cha Uhamiaji katika kijiji au Makao Makuu ya Tarafa ya Lukumbule?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Tunduru Kusini kulikuwa kuna vituo vitatu, Kituo cha Nalasi, Masuguru na Lukumbile lakini kwa bahati mbaya hiki kituo kimoja kilikuja kikatiwa moto baada ya kutokea machafuko ya wananchi. Hata hivyo, baada ya Serikali kuona umuhimu sasa wa kuwepo kituo ili sasa kuimarisha hali ya ulinzi pale, Serikali ikashusha Waraka kwa Halmashauri ya Wilaya ya Tunduru ili sasa watusaidie kujenga kile kituo hili eneo la Lukumbile. Hivi ninavyokwambia tayari kituo kimeshaanza kujengwa na kimeshafikia katika hatua ya lenta. Sasa kikubwa tu nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara tunaenda kutengeneza mazingira sasa ya kuona namna na kupitia umuhimu wa kuwepo kituo hiki ili sasa tuweze kuweka kituo hiki ili wananchi waweze kuishi katika mazingira ya usalama zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali la pili, hakuna Serikali yoyote duniani ambayo inapenda wananchi wake wapate tabu; wanyanyaswe, wapigwe, wadhulumiwe. Sasa kitu ambacho nataka nimuahidi Mheshimiwa Mbunge ni kwamba, kutokana na umuhimu wa suala hili tunakwenda kuona namna ambavyo tutakapotengeneza bajeti yetu hii Wilaya ya Tunduru hasa katika hii sehemu ambayo wanahitaji Kituo hiki cha Uhamiaji tutaipa kipaumbele ili tuone namna ambavyo tunaweza tukapata kituo cha uhamiaji hapa ili wananchi waweze kuepukana na huo usumbufu. Ahsante.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi hii ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu na takwimu zilizotolewa na Serikali, ukweli ni kwamba kutoka ngazi ya Mkaguzi Msaidizi kwenda Mkaguzi kamili inapaswa kufanyika ndani ya mwaka mmoja mpaka miaka miwili. Je, Mheshimiwa Waziri anayo taarifa kwamba kuanzia mwaka 2015 mpaka muda huu ambapo nimesimama mbele ya Bunge hili Tukufu kuna Wakaguzi Wasaidizi ambao hawajapandishwa madaraja?

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, Mheshimiwa Waziri atueleze hapa ikiwa anazo hizo taarifa ni kwa nini basi hao Wakaguzi hawajapandishwa madaraja?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Agnesta Lambert Kaiza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, si kweli kwamba tangu 2015 mpaka hapa tulipo watu hawajapandishwa madaraja. Kama ataangalia kwenye jibu langu la msingi nilitoa takwimu ambazo zinaonyesha kwamba kuna watu walipandishwa madaraja.

Mheshimiwa Spika, kingine nimfahamishe tu Mheshimiwa kwamba ni vizuri wakapata nafasi wakaipitia hii PGO (Police General Order) itawasaidia kujua baadhi ya taratibu ambazo zinatumika kupandisha madaraja. Kuna mambo ya msingi huwa yanaangaliwa, siyo kwamba watu wanapandishwa tu kwa sababu hawajapandishwa muda mrefu. Kwanza, lazima kipatikane kibali cha kupandisha majaraja. Pili, tunaangalia pia uwezo wa kiuongozi wa yule ambaye anatakiwa kupandishwa daraja. Tatu, tunazingatia zaidi vigezo vya kimaadili kwamba tunayekwenda kumpandisha cheo ana maadili gani katika kutumikia Taifa hili. Nne, tunaangalia kama hana mashtaka mengine. Tano, huwa tunaangalia na bajeti maana tukimpandisha cheo lazima tumpandishie na mshahara wake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa afahamu kwamba utaratibu ndiyo huo lakini tumeanza na tumepandisha madaraja mbalimbali kwa watumishi wa Jeshi la Polisi kama ambavyo taratibu zimeeleza.
MHE. NAJMA MURTAZA GIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, kwanza niipongeze Serikali kwa jitihada inazochukua katika kupiga vita ukatili wa watoto kwa suala la ubakaji. Hata hivyo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la kwanza litalenga kwenye majibu ambayo ameyatoa Mheshimiwa Naibu Waziri kuhusiana na tafiti ambyao amefanya na kututaka sisi sasa Wabunge pamoja na wananchi kwa ujumla kuweza kusaidia katika kutatua changamoto hizi.

Swali langu liko kwamba, je, ninyi kama Serikali mmejipangaje kuhakikisha kwamba vitengo vyote vinavyoshughulikia masuala ya sheria na kutoa haki vinashirikiana kikamilifu ili kuweza kutokomeza masuala haya ambayo mmeyatafiti?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili ni kuhusiana na Sheria Namba 21 ya Mtoto ya mwaka 2009. Sheria hii imeweka wajibu na jukumu la wazazi ama walezi kuweza kuwalinda watoto dhidi ya ukatili ikiwemo hili la ubakaji.

Je, mmekwama wapi katika kutekeleza sheria hii kiasi kwamba tunaona hakuna mzazi au mlezi anayeweza kuchukuliwa hatua pale ambapo mtoto anapatikana na makosa haya tukizingatia ndoa zinavunjika kwa wingi na watoto wanatelekezwa na inasababisha kufanyiwa vitendo hivyo vya ukatili, lakini pia wale wazazi ambao wanabaki, akina baba wanaweza kufanya vitendo hivyo vya ukatili kwa watoto wao wenyewe. Je, Serikali inasemaje kuhusiana na hilo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mbunge, Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza lilikuwa linasema kwamba, je, Serikali ina mpango gani au je, kuna jitihada gani nyingine ambazo zimechukuliwa na Serikali, ili kuhakikisha kwamba, tunatokomeza vitendo hivi. Kama Serikali tumechukua jitihada nyingi na tumechukua jitihada mbalimbali, lakini bado tunaendelea kuchukua jitihada ya kwanza ikiwemo ya kuendeleza kutoa elimu kwa jamii kwa sababu, tunaamini jamii ikipata elimu ya kutosha kwenye masuala haya maana yake masuala haya yanapungua au yatamalizika moja kwa moja. kwa hiyo, kama Serikali tumeanza kutoa taaluma kwanza kupitia kwenye madawati ya kijinsia ambayo mara nyingi yapo katika Jeshi la Polisi, tunayatumia yale kutoa taaluma hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine tunao hawa para legals, wasaidizi wetu wa sheria ambao wako huko, wanatusaidia kuipa jamii taaluma. Pia tunavitumia vyombo vya habari kuhakikisha kwamba, taaluma inafika kwa jamii, lakini kizuri zaidi tunaenda kutengeneza mazingira ya kuipa nguvu sheria hii Namba 21 ya mwaka 2009 ili kuhakikisha kwamba, sheria inafuatwa na wananchi kwa kiasi kikubwa jamii inapungukiwa na matendo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine la pili ameuliza kwamba, sheria hii inakwama wapi? Naomba pia kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kwamba, wakati tunaipitia sheria hii tumegundua kwamba, sheria hii ipo kimadai zaidi rather than kijinai. Sasa ukitazama unakuta kwamba, watu wanaweza wakafanya vitendo hivi wakitegemea kwamba, wao watafunguliwa kesi zaidi za madai na kwa sababu, madai si analipa. Kwa hiyo, sasa unakuta haiko kijinai zaidi. Kwa hiyo, unakuta sheria ndio maana unafika wakati utendaji wake wa kazi unakuwa haupo vizuri sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ni ugumu wa wananchi kwenda kutoa ushahidi, ugumu wa mashahidi. Ukimchukua mtu akitoa ushahidi huko nyumbani ukikaa naye atatoa ushahidi vizuri tu, tena atatoa ushahidi maana yake ambao uko evident, lakini kesho twende mahakamani ndio inakuwa ngumu. Sasa na mahakama nayo ikiwa siku mbili, tatu, mara nne tano umeitwa hujaenda kutoa ushahidi maana yake mahakama inatoa uamuzi kwa upande mmoja. Kwa hiyo, upo ugumu kwenye utoaji wa ushahidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine sasa wanafamilia, wanamalizana tu kienyeji. Jambo limetokea kwa sababu, baba mkubwa, baba mdogo wanamalizana huko mwisho wa siku huku sheria inakuwa haipewi nguvu. Nakushukuru.
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kuwa Serikali imekiri kuleta Sheria ya Makosa ya Jinai ya mwaka 2009 Bungeni, je, Serikali haioni umuhimu wa kuleta mabadiliko ya sheria ambayo inawafanya makosa ya jinai kwa wafungwa waliokaa mahabusu kwa muda mrefu iletwe ili iweze kupunguzwa muda wa kukaa muda mrefu kwa mfano wale wafungwa Masheikh wa Uamsho?

Swali la pili, Serikali haioni umuhimu sasa badala ya kuwekeza kujenga mahabusu mpya nyingi iwekeze kwa kumsaidia DPP kujenga uwezo wa kusimamia kesi ambazo kwa muda mrefu zimekuwa mahakamani, ushirikishwaji na ujibuji wa maswali yao wakienda mahakamani inakuwa bado upelelezi unaendelea?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi sasa naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khatib Said Haji kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza lilikuwa linasema je, hatuoni haja sasa ya kuweza kufanya baadhi au mabadiliko katika hii Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai?

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nataka nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba akipata muda akiipitia sheria hii atagundua kwamba tayari kuna baadhi ya maeneo yalishafanyiwa marekebisho kitu ambacho sasa kimeelekea katika kupunguza kwa asilimia kubwa huu mrundikano. Kwa mfano, ukiangalia katika kifungu cha 170; ukiangalia kifungu cha 225 na ukiangalia katika maeneo ya 163 na hayo na baadhi ya mengine ni maeneo tuliyoyafanyia marekebisho ili kuona tunapunguza hii changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kingine tunapotaka kufanya marekebisho ikiwa addendum ama amendment ya sheria kuna mambo ya msingi tunakuwa tunayaangalia. Kwanza tunaangalia applicability ya ile sheria, je, ipo applicable? Ikiwa kama sheria ina tatizo katika utekelezaji wake pale tunasema sasa tuna haja ya kufanya mabadiliko.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hilo halitoshi tunakuwa tunaangalia na mahitaji ya jamii kwa wakati ule, sasa kikubwa mimi niseme tu kama wanahisi au Mheshimiwa Mbunge anahisi kwamba kuna haja basi tutakwenda kukaa tuipitie tena tuone, pamoja na mabadiliko tuliyokwisha kuyafanya tutakwenda kukaa ili tuone kwasababu lengo na madhumuni ni kuhakikisha kwamba changamoto za mrundikano wa majalada na mrundikano wa mahabusu katika mahakama na wafungwa inapungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama hilo halitoshi swali la pili Mheshimiwa Mbunge amesema kwamba tuone namna ya kuwapa uwezo au kwa nini tusifanye maarifa DPP tukampa kazi ya kuweza kufanya upelelezi ili mambo yakaenda. Kazi ya kufanya upelelezi kwa mujibu wa taratibu kuna vyombo maalum vinavyohusika kufanya upelelezi. Wenye kufanya upelelezi ni polisi na siyo polisi wote kuna vitengo maalum vya kufanya upelelezi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenye kufanya upelelezi labda ni watu wa TAKUKURU, wenye kufanya upelelezi labda watu wenye kazi maalum tukisema leo DPP tunampa kazi ya kufanya upelelezi tunamuongezea jukumu lingine na usije ukashangaa akasema na kamshahara nako kapande. Mimi niseme tu kwamba kwa kuwa haya mashauri yametolewa tunayachukua tunakwenda kuyafanyia kazi nakushukuru.
MHE. VEDASTUS M. MATHAYO: Mheshimwa Spika, ahsante. Naomba kumuuliza Mheshimwa Naibu Waziri maswalli mawili ya nyongeza pamoja na majibu mazuri aliyoyatoa. Swali la kwanza; ni ukweli usiopingika kwamba kama alivyosema ziko pikipiki ambazo labda wakati mwingine zinaokotwa na zinapelekwa pale. Kwa maana yake ni kwamba hakuna jalada lolote llinalofunguliwa kwenda mahakamani na matokeo yake pikipiki na magari kama hayo yanaweza kukaa zaidi ya miaka kumi.

Je, tunakubaliana kwamba sasa viendelee kukaa hapo na kuozea hapo au ni vizuri vikafanyiwa utaratibu mwingine ili hiyo fedha ikapatikana kwa ajili ya maendeleo ya nchi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili; wakati tunaunda Sheria ya kuruhusu bodaboda ili waweze kufanya kazi na kupata ajira kilichotokea ni kwamba zilezile faini zilizokuwa zinatumika kwenye vyombo vya usafiri ndio zilizochukuliwa na wakaanza kubandikwa bodaboda, lakini ikumbukwe kwamba bodaboda anabeba abiria mmoja, akikutwa na kosa analipa Shilingi elfu thelathini basi lenye abiria 60 akikutwa na kosa hilo hilo analipa elfu thelathini. Sasa napenda kujua ni lini Serikali itabadili hizi adhabu inayolingana na bodaboda ambayo ni ya chini ukilinganisha na adhabu iliyopo ambayo pia inatozwa kwa magari?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Vedastus M. Manyinyi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ameulizia, je, Serikali haioni haja ya bodaboda hizi ambazo zimelundikana katika vituo hivyo vya polisi basi ziuzwe au zipigwe mnada ili sasa Serikali iweze kujipatia mapato? Jibu ni kwamba, uwepo wa pikipiki hizi kwenye vituo hivi kama nilivyosema katika jibu langu la msingi ni kutokana na sababu tofauti. Ukiziona pikipiki zimekaa kwenye Kituo cha Polisi usifikirie kwamba zimekaa kwa muda mrefu kwa sababu, utaratibu ni kwamba baada ya miezi sita endapo mwenye pikipiki yake asipokwenda kwenda kuikomboa pikipiki ama kulipa faini au taratibu nyingine akaziruhusu zikaendelea, maana pikipiki ile itaendelea kubakia pale.

Mheshimiwa Spika, baada ya miezi sita itaenda kupigwa mnada. Kwa hiyo inawezekana pikipiki hizo ambazo mnaziona kwenye Vituo vya Polisi ni kutokana na kwamba muda wake haujafika. Kwa mujibu wa taratibu hatutaweza kuipiga mnada ama kuiuza pikipiki ya mtu bila ya muda uliokusudiwa ama uliowekwa katika utaratibu kuwa haujafika.

Mheshimiwa Spika, utaratibu upo na kanuni na sheria zipo; ukiangalia kwenye PGO, ile 304 ukiangalia kwenye kifungu cha (1), (2), (3), (4), (5) na kuendelea imeelezwa Jeshi la Polisi limepewa mandate au limepewa mamlaka ya kuuza na kupiga mnada endapo itazidi zaidi ya miezi sita. Kwa hiyo hizo pikipiki zilizopo huko ni kwa sababu muda wake wa kufanyiwa hivyo haujafika, utakapofika hazitaonekana hizo. Aidha, nipende kusema kwamba tuendelee kushirikiana kutoa elimu huko kwa vijana wetu ili wasiendelee kuzifikisha huko.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa swali la pili, anasema, basi litapakia watu zaidi ya 30 faini yake ni Shilingi elfu thelathini, bodoboda ambayo inapakia mtu moja faini yake ni Shilingi elfu thelathini; sasa Serikali haioni haja hapa sasa ya kufanya marekebisho? Serikali katika hili bado haijaona haya ya kufanya marekebisho ya hili. The way itakavyofanya marekebisho kwa sababu nilivyomfahamu Mheshimiwa tushushe, maana kama basi watatoa shilingi 80,000, maana yake bodaboda watoe shilingi 10,000.

Mheshimiwa Spika, hizi Shilingi elfu thelathini ambazo zimewekwa bado matukio yanaongozeka na lengo letu sio kuwakomoa wananchi ama kuwakomoa vijana watumiaji wa bodaboda na pikipiki, lengo ni watu kufuata sheria kuepuka na kupunguza idadi ya ajali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka kufika Disemba, 2020 ajali za bodaboda ni 164; waliokufa ni 134 ambao wamekuwa injured 129 tu, tukizipunguza hizi tukisema sasa tuweke shilingi elfu kumi, vijana watazidi kufanya zaidi na hapo lengo na madhumuni ana uwezo wa kulipa Shilingi elfu kumi. Kwa hiyo tu niseme hatufanyi hayo kwa ajili ya kuwakomoa, tunafanya ili watu wafuate.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna utaratibu, nimekuwa nauona sana kule Zanzibar, vijana wanajazana kwenye magari makubwa yanaitwa mafuso, wanakwenda ufukweni huko muda wanaorudi huko wanarudi na bodaboda pikipiki hazipungui 30 au 40 njiani, lazima ajali inatokea, sasa kwa sababu analipa shilingi elfu kumi watafanya vyovyote kwa hiyo.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba tunayachukua mawazo tutakapo ona haja ya kufanya mabadiliko ya hii sheria tutafanya lakini kwa sasa naomba tuwe na hili.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha. (Makofi)
MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, swali langu lilikuwa linaendana na haya mahusiano kati ya bodaboda na Trafiki na kule Makete mahusiano ya bodaboda na traffic ni kama Refa ambaye yuko uwanjani ana kadi nyekundu tu, mahusiano yao ni mabaya sana kwa kiwango ambacho Traffic wanatoza faini ya shilingi laki mbili, tofauti na utaratibu wa kawaida. Tumejaribu kufanya vikao vya negotiation kati ya sisi na watu wa Trafiki lakini imeshindikana. Pili, Traffic wanafuata bodaboda wangu mashambani kule Matamba, kule Makete, kitu ambacho ni kunyume na utaratibu. Sasa je, Mheshimiwa Naibu Waziri anatupa kauli gani na maelekezo yapi kwa Trafiki Mkoa wa Njombe hususani Wilaya ya Makete dhidi ya vitendo viovu ambavyo vinafanywa na wao dhidi ya bodaboda wa Makete? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba sasa kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Sanga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utaratibu wetu kwenye PGO na utaratibu uliowekwa kwenye ile sheria au kanuni ya 168 ambayo imefanyiwa mabadiliko mwaka 2002, umesema ni Shilingi elfu thelathini, sasa kama kutatokezea askari au yoyote ambaye anayehusika na hili akawatoza watu zaidi ya kiwango kilichowekwa maana huyo anafanya kosa kwa mujibu wa taratibu kwa mujibu wa Sheria.

Mheshimiwa Spika, watu kuwafuata huko, unajua mtu anapokuwa mhalifu kwa mujibu wa utaratibu vyombo vinavyohusika kumkamata vina uwezo wa kumfuta popote alipo endapo amefanya makosa, lakini sasa hiyo namna ya kumfuata nayo ina utaratibu wake. Kwa hiyo, niseme tu kwamba, kama kutakuwa kuna askari amechukua zaidi ya hizo, maana huyo anavunja sheria, nadhani Mheshimiwa tushirikiane katika hili kuweza kuwakamata na kama tunawajua tuwalete katika ofisi yetu, tujue namna ya kuwashughulikia kwa mujibu wa taratibu. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. SAADA MONSOUR HUSSEIN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Pia nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri.

Mheshimiwa Spika, swali langu la kwanza, je, ni njia zipi kama Serikali mnazitumia kuwajulisha wale ambao hadi leo hawajapatiwa vitambulisho vyao kwenye vituo vya NIDA?

Mheshimiwa Spika, je, Serikali inatambua kuwa kwenye ofisi za NIDA kuna uhaba wa watumishi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge Saada Mansour Hussein, lakini pia nataka kutumia fursa hii kumpongeza sana kwa kazi nzuri na kubwa ambayo anaifanya katika Mkoa wa Kaskazini ya kuhakikisha kwamba akina mama au wananchi, lakini zaidi akina mama na watoto wanaishi katika mazingira mazuri zaidi.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza ni njia zipi ambazo tunazichukua kama Serikali kuhakikisha kwamba wale ambao hawajaenda kuchukua vitambulisho vyao taarifa zinawafikia.

Mheshimiwa Spika, kwanza nataka nichukue fursa hii, niwashukuru wananchi na viongozi kwa kuwa wametambua kwamba bado kuna baadhi ya wananchi hawajaenda kuchukua vitambulisho vyao mpaka muda huu, badala yake wanakaa wanalaumu Serikali. Kwa hiyo kikubwa ambacho nataka niseme ni kwamba, zipo njia nyingi ambazo huwa tunazitumia kuwafikishia ujumbe au taarifa kwamba vitambulisho vipo na waje.

Mheshimiwa Spika, ya kwanza; huwa tunawatumia ujumbe mfupi, kwa wale ambao namba zao zipo hewani zinapatikana. Pia huwa tunawapigia simu kabisa kuwajulisha. Vile vile kupitia Ofisi za Wakuu wa Wilaya na kupitia Ofisi za Masheha na Watendaji huwa tunatoa taarifa hizo ili wananchi ambao wameshatengenezewa vitambulisho vyao, lakini hawajaenda kuvichukua, waende wakavichukue.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, nikiri kwamba, bado tuna changamoto ya rasilimawatu katika Ofisi zetu za NIDA, lakini nimwambie Mheshimiwa aendelee kustahimili, Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kupitia NIDA tupo katika mchakato wa kutengeneza mazingira ya kuajiri vijana, lengo na madhumuni, shughuli za NIDA ziweze kwenda vizuri.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina swali moja tu. Je, Serikali ina mpango gani wa kuendeleza kituo hiki kwa sababu kituo hiki ni chakavu, cha siku nyingi na kibovu. Sasa naiomba Serikali tufuatane, tuongozane na Waziri ili akajionee mwenyewe katika kituo hicho cha Bububu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwantakaje Haji Juma, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nimpongeze kwa juhudi kubwa anayoifanya na najua anataka kile kituo kifanyiwe ukarabati ili kiweze kutoa huduma kwa sababu jimbo lake ni jimbo ambalo lina harakati nyingi za kiutalii ambazo zinachangia pato kubwa la Taifa. Kwa hiyo harakati hizi sometime zinakuwa zinapelekea athari za kiusalama.

Mheshimiwa Spika, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa kwamba nipo tayari kufuatana naye kwenda kukagua kituo kile chumba kwa chumba, eneo kwa eneo ili kuona wapi panahitaji marekebisho na tuko tayari kama Serikali kukirekebisha kituo kile. Nakushukuru.
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Ningependa kuuliza maswali mawili ya nyongeza japo majibu walionipa angalau yanaridisha.

Swali la kwanza, natamani kufahamu; kwa kuwa magereza wao wamekiri bado uwezo wa kulisha mahabusu na wafungwa ni mgumu, upo kwa asilimia 54. Je, hawaoni sasa ipo haja ya hawa mahabusu kuweza kushirikishwa kuzalisha chakula chao tu kwa sababu maandiko yanasema kila mtu atakula kwa jasho lake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili natamani kufahamu; tunafahamu kabisa Magereza changamoto ya magodoro ni kubwa sana. Katika changamoto hiyo, Serikali inawajibika kuhakikisha magodoro yanakuwepo kule, lakini hali bado ni ngumu; na tunafahamu kuna taasisi nyingi sana zinazokuwa zinahitaji magodoro kama shule na Serikali haiwapatii:-

Je, Serikali haioni iko haja sasa ya mahabusu au wafungwa wote wanaokuwa wanafungwa wakawa na kigezo cha kwenda na magodoro yao ili kuweza kupunguza changamoto ile kwa sababu sio wote wanashindwa kuwa na godoro hilo kuliko kuiongezea Serikali mzigo? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Neema kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Kanuni au Sheria, hakuna eneo ambalo linakataza kwamba watu kuingia na vitu wanavyovitaka katika Magereza, lakini sasa sababu mbili ndizo ambazo zinatufanya mpaka tufike hatua ya kusema kwamba haiwezekani kila mtu aingie na kitu chake Gerezani. Sababu ya kwanza, moja ni busara ya Jeshi la Magereza kama Jeshi la Magereza. La pili, ni sababu za kiusalama.

Mheshimiwa Spika, unapochukua kitu ukakiingiza kwenye Magereza, maana yake kinaweza kikachomekwa kitu kingine ndani yake ambacho kinaweza kikaja kuwadhuru wengine. Ndiyo maana hata ukifika wakati ukitaka kuleta chakula au dawa au kitu kingine, lazima tukithibitishe tukihakikishe na tujue kwamba hiki kina usalama kwako, kwetu tunaokipokea na kwa yule ambaye anakwenda kukitumia. Kwa hiyo, suala la kila mtu aingie na godoro lake, pazito kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine tunaweza tukajikuta tunatengeza tabaka kwamba kuna mtu anaweza kuingia na godoro lake na mwingine akashindwa. Kwa nini sasa na mahabusu nao wasishiriki katika shughuli za uzalishaji? Mahabusu na wafungwa wote ni binadamu, lakini hata akiitwa mfungwa, maana yake kesi yake imeshakuwa held, kwa maana ya kwamba imeshahukumiwa aende jela miaka mingapi? Kwa hiyo, yule tunayo sababu ya kumwambia sasa nenda kalime, nenda kazalishe kwa ajili ya kutengeneza mazingira ya gereza. Sasa huyu mahabusu bado kesi yake haijahukumiwa kwa hiyo, yupo pale. Kusema tumchukue tukamfanyishe kazi, tukamlimishe bado kidogo busara hiyo hatujafikia. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. OMAR ALI OMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri, kwanza naipongeza Serikali ya Awamu ya Sita kwa kuendelea kutupa majibu ya uhakika ya kupata ajira kwa vijana wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza;

Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, suala la ajira kwa vijana wa Jeshi la Polisi, hasa wa Mkoa wa Kaskazini Pemba, Serikali ina mpango gani wa kupeleka askari 150 katika Mkoa wa Kaskazini Pemba ambapo ndiyo tatizo kubwa kwa sasa hivi?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili ni kwamba; Jeshi la Polisi linapoajiri vijana kupitia Jeshi hili kuna tatizo/ changamoto moja kubwa kabisa; vijana wengi wanaondoka kutoka mkoa mmoja kwenda mwingine kuomba ajira ya Jeshi la Polisi,

Je, changamoto hii wamejipangaje kuhakikisha kwamba vijana wa Mkoa wa Kaskasini Pemba ndio wale wanaohusika hasa kutokana na sifa walizonazo kajiriwa katika Jeshi la Polisi? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimwa Omar Ali Omar kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie fursa hii kwanza kumpongeza kwa kuwa Mheshimiwa Omar siyo tu amekuwa mwakilishi ama Mbunge wa Jimbo la Wete, lakini pia amekuwa anafanya kazi na kuusemea mkoa wake kwa ujumla katika mambo mbalimbali yanayohusu masuala ya siasa, uchumi na mambo mengine.

Mheshimiwa Spika, kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba nafasi hizi zimekuja na zitakwenda katika kila mkoa. Na zitapita katika kamati za ulinzi na usalama kama utaratibu ulivyokuwa umepangwa. Lakini kikubwa nimwambie kwamba idadi ya nafasi alizozitaja zinaweza zikaenda mahali ambapo patakuwa pana uhitaji zaidi.

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo yana uhitaji zaidi. Kwa mfano kuna maeneo yana idadi kubwa ya watu (wananchi), kwa sababu utaratibu ulivyo ni kwamba askari mmoja analinda raia kuanzia 350 mpaka 400, kwa hiyo ikiwa mahali pana watu wengi panaweza pakapelekwa idadi hiyo. Lakini pia tutaangalia na crime rate (hali ile ya vitendo na matukio ya uhalifu ya mara kwa mara) pia yatatupa sisi impetus ya kuona wapi tuangalie itakavyowezekana.

Mheshimiwa Spika, lakini kikubwa nimwambie Mheshimiwa, kwamba katika Mkoa wa Kaskazini Pemba, nafasi hizi zitakwenda na vijana wataomba na Serikali itaendelea kutekeleza azma yake ya kuwaahidi wananchi na kuwatekelezea. Asiwe na wasiwasi wananchi/vijana wake wataajiriwa.

Mheshimiwa Spika, kuhusu changamoto ya vijana kutoka mkoa mmoja ama wilaya moja kwenda nyingine kuomba hizi nafasi. Kiutaratibu sifa inayokuja anatakiwa awe Mtanzania, haikusema kwamba atoke Pemba au Unguja au wapi. Kwa hiyo anaweza akatoka sehemu moja akaenda nyingine.

Mheshimiwa Spika, lakini kikubwa tuwaambie kwamba watakaosimamia nafasi hizi wahakikishe vijana ambao wako katika mkoa husika wapate hizi nafasi ili lengo na madhumuni vijana waweze kupatiwa ajira kama ambavyo Serikali iliwaahidi wakati wa kampeni. Nakushukuru.
MHE. ABDUL-HAFAR IDRISSA JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa majibu ya kuridhisha kiasi ya Naibu Waziri, lakini vitendo vya udhalilishaji na uhalifu katika Wilaya ya Magharibi “A” ambapo Jimbo langu la Mtoni lipo, lakini pia na kituo hicho cha polisi tunachokizungumzia kipo, vimekuwa vikiongezeka sana.

Sasa je, nini kauli ya Serikali katika wakati huu wa vitendo vikiongezeka na kituo kimefungwa nini kauli ya Serikali juu ya mapambano yake ama inafanya nini kuhakikisha kwamba vitendo hivi vya uhalifu na udhalilishaji unapungua?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abdul-Hafar Idrissa Juma, Mbunge wa Jimbo la Mtoni, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimuambie Mheshimiwa Abdul kwamba nipo tayari kufuatana na yeye kwanza kwenda kukiona kituo hicho, lakini pia nipo tayari kwenda kukaa na uongozi wa Jeshi la Polisi katika Mkoa wa Mjini ili lengo na madhumuni kuweza kufanya nao mazungumzo, ili ikiwezekana baada ya kujiridhisha tuone namna ambavyo tunaweza tukakifungua kituo hiki na kikaendelea kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia nipo tayari kwenda kukaa na wananchi kuweza kuwaambia maneno mazuri ambayo yatawapa imani ya kuendelea kuwa amani na salama na utulivu katika Jimbo lao. Lakini kikubwa nimuambie kwamba hili suala lake aliloliuliza la kuongezeka kwa matukio haya ya udhalilishaji katika Mkoa huu, katika Jimbo lake na katika Wilaya hii, Serikali tuna mipango mingi ambayo tumeshaanza kuifanya. Lakini kubwa nimuambie kwamba kwanza tunakwenda kuongeza nguvu kwenye masuala mazima ya ulinzi shirikishi. Ulinzi ambao unawapa nafasi wananchi wenyewe kushiriki katika ulinzi huu wa wananchi wao binafsi na hapa nataka nichukue fursa hii, nimpongeze sana Mheshimiwa Abdul-Hafar amekuwa anafanya kazi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza amewatafutia kituo hawa walinzi shirikishi, lakini kubwa amewatafutia vifaa vya ulinzi kwa ajili ya kufanya doria zao. Lakini pia anafika wakati anawagawia hata posho ili lengo na madhumuni shughuli za ulinzi katika Jimbo lake ziendelee. Lakini kingine ni doria, misako na operesheni mbalimbali tunaziendesha katika Jimbo hili, ili lengo na madhumuni wananchi waishi kwa amani. Lakini kikubwa ziara za Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya na Mikoa tutajitahidi tuziongeze katika Jimbo hili na maeneo mengine ili lengo na madhumuni wananchi waweze kujua wajibu wao na waishi kwa ulinzi, amani na utulivu. Nashukuru.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Niishukuru Serikali kwa mpango wake wa kujenga mahakama kule Mbulu, Kituo cha Polisi cha Wilaya ya Mbulu iko ndani ya hifadhi ya barabara ya mita 30 na kwa kuwa barabara hiyo ya kwenda Haydom iko kwenye mpango wa kutangazwa tender kwa kiwango cha lami. Je, Serikali ni lini itakuja kujenga Kituo cha Polisi cha Wilaya ili kuondoa kadhia hii ambayo itasababisha huduma kusimama?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zacharia na ninajibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali tunatambua changamoto ya ulinzi au changamoto ya ukosefu wa Kituo cha Polisi hilo eneo ambalo Mheshimiwa amelitaja, lakini kikubwa nimuambie kwamba moja ya miongoni mwa kazi kubwa ya Serikali ni kuhakikisha kwamba inawapelekea wananchi huduma za ulinzi na usalama. Nimhakikishie mbele ya Bunge lako hili kupitia Wizara yetu, Kituo cha Polisi Mbulu kitafika na wananchi wataendelea ku- enjoy ama kupata huduma za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. TUMAINI B. MAGESSA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani, naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza, kwa vile sasa Kituo cha Geita sasa kitakuwa kinahudumia mkoa mzima, nami ninachojua ni kwamba pale Geita hata gari la zimamoto halipo: Je, ni lini Geita itapata gari la Zimamoto ili iweze kuhudumia mkoa mzima kutoka kwenye center moja ya Geita? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa vile kutoka Geita ni mbali na Katoro, ni lini sasa Kituo cha Polisi cha Geita kitapewa gari la Polisi ili liweze kuwahudumia wananchi wakati wakisubiri huduma ya gari la zimamoto kutoka Geita ili mali zao zisiporwe wala kuharibika baada ya moto kutokea? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mji wa Geita kuna jumla ya magari manne ya zimamoto. Magari haya ni mazima na yanafanya kazi katika mkoa huo. Kwa bahati nzuri, pia sasa Serikali imeshafikiria kupeleka gari la zimamoto katika mji mdogo wa Katoro. Kitu cha msingi ambacho namwomba Mheshimiwa Mbunge, aendelee kustahimili kidogo, Serikali tumo mbioni kupeleka gari la zimamoto katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba wakati wao wanaendelea kustahimili, zipo njia mbadala ambazo tunazitumia kuhakikisha kwamba itakapotokea majanga hasa ya moto na mengine, wananchi hawa wanaweza kupata msaada wa haraka. Hivi karibuni tulifunga mkataba ama makubaliano na wale skauti, kwamba watusaidie kuendelea kutoa taaluma, washirikiane na Jeshi la Zimamoto ili kuhakikisha kwamba taaluma inaenea na majanga yanapotokea wanaweza kupata msaada wa haraka. Sisi kama Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto pia tunaendelea kutoa taaluma. Kikubwa ambacho tumesisitiza hasa kwa Jeshi la Zimamoto, waweze kuwahi kwenye matukio kwa haraka panapotokea majanga haya.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili la Mheshimiwa, ni lini sasa tutapata gari la Polisi ambalo litakwenda angalau kuweza kutoa huduma? Katika Mji Mdogo wa Katoro, Kituo cha Polisi cha Katoro tayari gari la Polisi lipo, ipo gari ya One Ten, ambayo inatumika, sema tu, kwa kweli gari ni ya muda mrefu, limechakaa. Tunachowapongeza Jeshi la Polisi, Geita wameshaomba magari katika Jeshi la Polisi ili waweze kupelekewa magari hayo yaweze kuwasaidia katika harakati mbalimbali za ku-serve maisha ya jamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nashukuru.
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, naomba nimjibu maswali mawili ya nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, je, katika bajeti ya mwaka huu wa fedha kumetengwa fedha kwa ajili ya ujenzi wa ofisi hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Je, Mheshimiwa Naibu Spika uko tayari kuambatana ili twende ukajionee katika eneo hilo mwenyewe kwa macho yako hali halisi ya kusaidia kuhamasisha wananchi wako wa Mkoa wa Kusini Unguja, ili na wao wajue kwamba, wewe Naibu wao unafanya kazi vizuri? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kama ambavyo nimeeleza kwenye jibu langu la msingi, kukwama kwa kituo hiki kulikuwa kunasababishwa na upungufu wa fedha ambao sasa unatokana na ufinyu wa bajeti. Je, naulizwa, katika bajeti hii tumeingiza hiyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie kwamba, katika bajeti hii haikuingizwa, lakini nimuahidi tu kwamba, katika bajeti ijayo tutajitahidi hii Ofisi ya OCD Wilaya ya Kusini Unguja na ofisi nyingine na maeneo mengine ambayo yana uhitaji wa vituo hivi tutajitahidi tuhakikishe kwamba, tunapeleka au tunaendeleza ujenzi. Hasa ule ujenzi ambao umekwama wa vituo vya polisi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali jingine je, nipo tayari kuambatananaye mama yangu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nikwambie. Kwa ridhaa kabisa niko tayari kuambata na Mheshimiwa Mbunge tuende huko tukaangalie hilo eneo. Na itakuwa vizuri kwa sababu, tukifika huko tutawakusanya wananchi…

MBUNGE FULANI: Sio wewe.

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: …lakini
pia tutakaa na wadau ili kuhakikisha kwamba, tunawashajihisha kujenga kituo hiki, ili wananchi wa maeneo hayo, hasa maeneo ya Makunduchi, Kizimkazi, Mtende, Bwejuu, Paje na Jambiani na maeneo ya karibu waweze kupata huduma za ulinzi na usalama kama wanavyopata wananchi wengine. Nakushukuru.
MHE. DKT. CHRISTINE G. ISHENGOMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipatia swali la nyongeza:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Kisaki ambacho kiko Morogoro Vijijini kwa umuhimu wake kina matatizo ya usafiri. Je, ni lini kitapewa usafiri angalau pikipiki?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli nikiri kwamba, bado tuna changamoto ya usafiri hasa katika maeneo ya vituo vya polisi, ikiwemo pikipiki na gari na aina nyingine za usafiri. Sasa nimwambie tu Mheshimiwa kwamba, aendelee kuvuta subira, Serikali kama Serikali tumo mbioni kuhakikisha kwamba, vituo vya polisi na maeneo mengine ambayo yanatoa huduma za ulinzi na usalama kwa wananchi tunahakikisha tunapeleka hivyo vyombo vya usafiri, ili sasa wananchi waweze kupata hizo huduma kama inavyotakiwa. Nakushukuru.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Suala la Mkoa wa Kusini Unguja ni sawasawa na suala la Mkoa wa Kaskazini Unguja. Je, ofisi iliyokuweko Mkokotoni itamalizika lini? Maana huu mwaka wa tano unakwenda wa sita, bado kumalizika?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli ofisi ile ipo kwa muda mrefu na ujenzi wake ulikwama hapa katikati, lakini nimhakikishie tu kwamba, Mheshimiwa Mbunge ukarabati na kuendelea kumalizika ujenzi wa jengo lile sasa hivi umo mbioni. Na kama atakuwa ameanza kupita kwa muda huu anaweza akayaona mabadiliko ya ujenzi ule.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwaombe wananchi, hasa wa Mkoa wa Kaskazini Unguja, jambo lao tayari lipo na linatekelezwa na muda si mrefu sana wataanza kutumia kituo kile na wataendelea kupata huduma za ulinzi na usalama katika maeneo yale, hasa ya Mkokotoni, maeneo ya Donge, maeneo ya Mkwajuni na maeneo mengine ya Mkoa wa Kaskazini Unguja. Ninakushukuru.
MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana; na mimi kwa niaba ya wananchi wa Biharamuro ningependa niongezee swali la nyongeza. Wilaya ya Biharamuro ni miongoni mwa wilaya kongwe kabisa za nchi hii lakini ukiingia katika mazingira ya polisi wa Biharamuro wanapoishi, bado wanaishi kwenye nyumba zilizojengwa na Mkoloni pale. Lakini mazingira ya kazi ni magumu wote mnajua kumekuwa na majambazi kule lakini vijana wale wanajitahidi kupambana nao usiku na mchana na hali yetu ni shwari kabisa.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa maswali niliyonayo ni mawili, ni lini tutajengewa kituo kipya cha Polisi, ikizingatiwa tayari hati iko pale na kiwanja kipo tayari? Lakini pili…

NAIBU SPIKA: Moja tu Mheshimiwa; moja tu.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa ruhusa yako, nijibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, naendelea kukiri tena kwamba bado tuna changamoto hasa kwenye usafiri, makazi na Vituo vya Polisi. Kwa kuwa, kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge amesema, tayari wana hati ambayo inawamilikisha wao waweze kujengewa eneo zuri waweze kupata jengo zuri ambalo litatoa huduma za ulinzi na usalama kwa wananchi, nimwambie tu kwamba aendelee kustahimili na mimi nalichukua hili tunakwenda kulifanyia kazi ili tuhakikishe kwamba katika eneo lake wanapata kituo kikubwa kizuri na cha kisasa ambacho kitaendelea kutoa huduma kwa wananchi na wananchi wakaendelea ku-enjoy hiyo huduma ya ulinzi na usalama katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru.
MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Napenda kumuuliza Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Je, ni lini nyumba za Askari wa Wilaya ya Kusini zitafanyiwa marekebisho kwasababu hali yake ni mbaya sana? Inafikia hatua kwamba baada ya kupigiliwa misumari hizo nyumba zimewekewa vipande vya matofali na mawe; kwa katika kipindi hiki cha mvua ni hali ngumu sana za wale askari. Je lini nyumba hizo zitafanyiwa marekebisho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Ravia Idarus Faina Mbunge wa Jimbo la Makunduchi kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, sikuwa na uhakika sana kama kuna nyumba zimewekwa mawe badala ya kuwekwa bati; lakini kubwa niseme kwamba hata katika bajeti ambayo tuliyonayo mwaka huu tayari ujenzi wa nyumba hizi umezungumzwa na hatua za ujenzi wa nyumba hizi upo mbioni. Na si nyumba hizi tu tayari tuna mpango wa kujenga kituo kikubwa cha Polisi katika Mkoa wa Kusini na nyumba za kukaa maaskari katika Mkoa wa Kusini. Kikubwa nimwambie Mheshimiwa Mbunge tuendelee kustahimili kidogo. Najua hili linamgusa na linamuuma kwasababu anawaona askari wanavyopata tabu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini binafsi nafahamu hili kwasababu huo Mkoa ni wa kwangu. Niseme tu kwamba ninalichukua hili tunakwenda kulifanyia kazi na nyumba za kukaa askari polisi Wilaya ya Kusini hasa Makunduchi zitapatikana Inshallah.
MHE. HAJI MAKAME MLENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali ambayo yametolewa, lakini bado nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kwa sababu ni muda mrefu sasa toka marehemu alipofariki na hadi leo hajapata na alikuwa ni mtendaji wa Jeshi la Polisi. Je, ni lini sasa Serikali itawapatia mafao yao hawa wahusika?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; naamini changamoto hii haiko kwa hawa tu, iko kwa watu wengi. Sasa je, Serikali inawaahidi nini wananchi wa Tanzania ambao wana matatizo kama haya juu ya kutatua tatizo hili? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Haji Makame Mlenge, Mbunge wa Jimbo la Chwaka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, je ni lini warithi wa marehemu watapata urithi wao. Baada ya kukaa na kupekua, kwanza tumegundua kwamba kweli marehemu alikuwa ni mtumishi wa Jeshi la Polisi, lakini changamoto kubwa ambayo tulifika tukakutana nayo, tulifika wakati tukakosa kujua ni nani anayesimamia mirathi ya marehemu. Sasa hii kwa kweli kwetu ikaja ikawa ni changamoto. Kwa kuwa tayari msimamizi wa mirathi hii tumeshampata, kikubwa tumwahidi tu Mheshimiwa Mbunge, tutashirikiana tuhakikishe kwamba mirathi au mafao haya yanapatikana kwa wale ambao wanasimamia mirathi hii.

Mheshimiwa Spika, kikubwa nimwambie binafsi niko tayari kwenda kukutana na huyo msimamizi wa mirathi na wengine wanaohusika na mirathi hii ili tuone namna ambavyo tunahakikisha watu hawa wanapata mafao yao au mirathi yao kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, lakini je ni nini sasa kauli ya Serikali katika suala hili au tuna mpango gani? Kikubwa ambacho nataka nimwambie Mheshimiwa cha mwanzo linapojitokeza jambo kama hili kwa wananchi wengine basi cha kwanza kabisa wateue au wafanye uchaguzi wa kuteua msimamizi wa mirathi, kwa sababu sisi la mwanzo tukutane na msimamizi. Yeye ndiye atakayesimamia na kutupa taarifa zote zinazohusika.

La pili, tuhakikishe kwamba wanawasilisha vielelezo kwa sababu hatutaweza kujua nini shida yake kama hakuna vielelezo vilivyowasilishwa vikiwemo vya taarifa ya kifo, vikiwemo labda kituo ambacho alikuwa akifanyia kazi, mkoa na kadhalika. Hivyo ni vitu ambavyo vitatusaidia sisi katika kuhakikisha kwamba anapata mirathi yake kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kingine wakati wanawasilisha hivyo vielelezo viende kwa watu husika. Wengine huwa wanawapa tu kwa sababu jirani yake ni askari atampa nipekee. Sasa pengine sio mhusika, matokeo yake sasa lawama zinakuja kwenye Serikali, Wizara au kwa Jeshi la Polisi.

Mheshimiwa Spika, kikubwa ambacho nataka niseme, ufuatiliaji wa mara kwa mara, kwa sababu na sisi tutakuwa tunalifuatilia lakini na wao sasa wawe wanalifuatilia kuhakikisha kwamba hii mirathi inapatikana kwa wakati. Nakushukuru.
MHE. ALOYCE J. KAMAMBA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Kutokana na kuwepo kwa mgogoro huo kwa muda mrefu, Mheshimiwa Waziri yuko tayari sasa kwenda eneo lenyewe la mgogoro ili aweze kujionea hali halisi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili. Je, ikidhihirika kwamba katika utaratibu huo wa kugawa mipaka kuna makosa ambayo yatakuwa yamejitokeza wakati huo: Serikali iko tayari kuchukua hatua kwa wale ambao watakuwa wamekiuka taratibu za utoaji mipaka?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, swali la kwanza la Mheshimiwa Kamamba ni: Je, nipo tayari kwenda katika eneo hilo ili nikajionee mwenyewe huo mgogoro? Nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge, ndani ya kipindi hiki cha Bunge la Bajeti nikipata nafasi ambayo itaniruhusu kuweza kwenda kwa sababu ni sehemu ya wajibu wangu kuyajua, kuyaona na kusikiliza changamoto za wananchi, nimhakikishie tu kwamba naenda kupanga ratiba na nitajitahidi nimjulishe tuweko pamoja ili kwa kushirikiana na maafisa kutoka hiyo Idara ya Wakimbizi, tuone namna ambavyo tunaenda kutatua hiyo changamoto ambayo kwa sasa wananchi inawakabili. Kwa hiyo, kwa ufupi ni kwamba, nipo tayari kufuatana naye kwenda katika eneo.

Mheshimiwa Spika, swali lingine ni: Je, ikidhihirika kama kuna makosa kuna watu wamefanya mambo mengine, mengine, Serikali ipo tayari kuchukua hatua? Serikali ipo kwa ajili ya kuwatetea, kuwasemea na kwa ajili ya kutatua changamoto za wananchi. Tumegundua kuna baadhi ya mambo yanafanywa na baadhi ya maafisa au baadhi ya watu ambayo yanavunja utaratibu na sheria katika maeneo haya. Kama Serikali tuko tayari kuchukua hatua ili kuhakikisha kwamba wengine wawe ni funzo na wasiendelee kufanya makosa hayo.

Mheshimiwa Spika, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba wakimbizi hawa tuliamua kuwapokea kwa sababu ya Mkataba wa Kimataifa ambao tuliukubali sisi wenyewe, kwamba ikitokea machafuko katika nchi fulani, basi kama wakija na tuki-prove kwamba kweli kuna tatizo, sisi tunawapokea.

Mheshimiwa Spika, pia tulikubaliana kwamba migogoro ikimalizika katika maeneo yao, sisi tupo tayari kuwarejesha katika maeneo yao kwa kushirikiana na mashirika na kwa kushirikiana na nchi zao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimwambie tu kwamba eneo hili ikitokea wakimbizi hawa wameondoka na ikawa hakuna machafuko, maana yake ni kwamba eneo hili tutalirejesha kwa Serikali, halafu Serikali itaona namna ya kufanya. Unless ikitokea fujo nyingine huko kwenye nchi za wenzetu ikawafanya wakimbizi waje, tutawapokea na kuwahifadhi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. JAFAR SANYA JUSSA: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza, je, ni lini Mheshimiwa Naibu Waziri atafanya ziara kuvitembelea vituo hivyo vya Jambiani na Paje na nyumba za askari wa Jeshi la Polisi Makunduchi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; je, ni lini Serikali italipatia Jeshi la Polisi, Wilaya ya Kusini gari kwa ajili ya doria?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sanya kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Sanya. Hakika amekuwa anafanya kazi kubwa sana ya kuwasaidia wananchi wa Jimbo la Paje hasa wa maeneo ya Jambiani, Paje, Bwejuu, Makunduchi, Kizimkazi, Mtende na maeneo mengine ya jirani ili kuhakikisha kwamba wanapata kwa utulivu na uhakika huduma za usalama na ulinzi katika maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikwambie tu ndani ya Bunge hili tumeshapanga na Mheshimiwa Sanya twende tukakabidhi mabati kwa ajili ya kuezeka Kituo cha Paje na fedha hizi zitatoka ndani ya mfuko wake. Kwa hiyo nimpongeze sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Sanya. Kwanza anauliza je, niko tayari kwenda kuangalia maeneo hayo? Nimejibu tu kwamba niko tayari na nimuahidi tu kwamba ndani ya Bunge hili la Bajeti tutapanga siku tuchupe mara moja twende tukakague, tukayaone hayo maeneo. Tukazione hizo hali na changamoto, halafu tujue namna ya kuzitafutia ufumbuzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini je, tuko tayari kutoa gari? Nimwambie tu kwamba awe na Subira, katika bajeti ijayo tutajitahidi Vituo vya Paje na Jambiani, Wilaya wa Kusini Unguja tuvizingatie zaidi katika kuhakikisha kwamba wanapata gari kwa ajili ya kufanya doria za ulinzi na usalama katika Jimbo lake. Nashukuru.
MHE. ZACHARIA P. ISSAAY: Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya miundombinu inayoikabili Jeshi la Polisi nchini inaikabili sana Wilaya ya Mbulu. Kituo cha Polisi katika Wilaya ya Mbulu kilijengwa mara baada ya uhuru, kwa sasa kina uchakavu mkubwa. Je, ni lini Serikali itatatua tatizo hili la uchakavu wa Kituo cha Polisi Wilaya ya Mbulu na makazi ya askari katika Wilaya yetu ya Mbulu? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu letu kama Serikali na Wizara ni kuhakikisha kwamba ulinzi na usalama wa nchi unaenea kila mahali. Hilo la kujenga vituo vya polisi na kuvipatia magari, yote ni sehemu ya jukumu na wajibu wetu. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge, awe na subira kidogo kwa sababu kasungura bado kadogo lakini kakija kakichononoka kidogo, basi hilo ni jambo ambalo linawezekana na tukipata fedha ya kutosha, basi tutampelekea kituo cha polisi na huduma nyingine za polisi katika Jimbo lake. Nashukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ningeomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. La kwanza, kwa vile tokea mwaka 2012 hadi leo hii ni miaka tisa imepita na idadi ya askari polisi imeendelea kupungua kutokana na askari wengi kustaafu katika maeneo ya Zanzibar.

Vilevile kuongeza kwa vitendo vya uhalifu katika baadhi ya maeneo, je, Mheshimiwa Waziri au Serikali haioni haja ya kuajiri askari zaidi katika maeneo ya Zanzibar na hasa mashambani ili kuweza kuziba hilo pengo kwa haraka? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali namba mbili, kwa vile askari jamii katika maeneo mbalimbali ya Zanzibar, wamekuwa ni msaada mkubwa na tayari kuna good practices katika baadhi ya maeneo. Je, Serikali haioni haja ya kuweza kupanua wigo wa askari jamii kwa kuwapatia mafunzo na motisha, ili kuweza kufanya kazi na kuweza kusaidia kupunguza vitendo vya uhalifu katika maeneo ya Zanzibar? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ili tuweze kufanya uajiri kuna mambo lazima tuyaangalie. La kwanza, lazima tuhakikishe kwamba, tumepata kibali cha kufanya uajiri kitu ambacho nataka nimuambie Mheshimiwa Mbunge, tumeshakifanya na tumo mbioni kuhakikisha kwamba, tunapata ruhusa ya kufanya uajiri.

Mheshimiwa Spika, lingine ili tuweze kufanya uajiri maana yake lazima tuhakikishe kwamba tuna bajeti ya kutosha kwasababu tukisha waajiri lazima tuwalipe. Sasa kikubwa ambacho nataka nitoe wito hapa leo kwa Waheshimiwa Wabunge, hasa Mheshimiwa Mbunge aliyeuliza swali na Waheshimiwa Wabunge leo tukijaaliwa hapa tunaenda kupitisha bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, tunaomba bajeti hii tuipitishe kwasababu, ndani ya bajeti hii imezungumzwa taarifa za ajira za vijana hasa kwenye jeshi la polisi. Kwa hiyo, nawaomba tupitishe hii bajeti ili sasa tuweze kufanya hizo harakati za uajiri.

Mheshimiwa Spika, nimeulizwa pia suala kuhusu namna bora ya kuweza kuwaboresha askari jamii. Nimuambie Mheshimiwa Mbunge kwamba hivi tunavyozungumza tayari Kamishna anayeshughulika na masuala ya askari jamii na ulinzi shirikishi Zanzibar kwanza, anachokifanya ni kutoa mafunzo kwa masheha na kamati za ulinzi na usalama za shehia na vijiji, ili lengo na madhumuni ni kuona namna bora ya kuweza kuwashirikisha wananchi katika kupata ulinzi. Lakini tayari kuna mfumo mzuri, mwongozo mzuri ambao umeshatolewa umeshaanza kutumika Unguja na Pemba soon inshalah utaanza kutumika. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kunipa nafasi kuuliza swali la nyongeza. Wilaya ya Liwale ni Wilaya ambayo iko mbali sana na makao makuu ya Mkoa ambako ni Lindi. Na pale Liwale hakuna kituo cha polisi kwa maana ya jengo hawana kabisaa, wanaishi kwenye nyumba ambayo ilipangwa na benki mpaka leo hii. Lakini, mwenyewe ni muhanga katika hili, mwaka huu mimi nimechomewa nyumba mbili na magari matatu wakati wa uchaguzi. Kimechangiwa sana na uhaba wa askari polisi na hatuna msaada wa karibu kutoka Liwale mpaka Nachingwea ni zaidi ya kilomita 120 mpaka Lindi zaidi ya kilomita 300. Sasa, je, Serikali ina mkakati gani kwanza, kutuongezea polisi Wilaya ya Liwale ikiwepo pamoja na majengo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwanza niko tayari kama ambavyo umenishauri kwenda kutembea Liwale, bahati mbaya kidogo sijafika Liwale. Lakini najitahidi katika kipindi hiki cha Bunge la Bajeti tunaweza tukatenga siku moja tukaenda Liwale kwenda kuangalia hiyo hali, halafu tutarudi tuje tuone sasa namna ya kufanya tathmini kuona namna ya kuweza kusaidia.

Mheshimiwa Spika, lakini, suala hili la uhaba wa askari mimi nadhani tuje pale pale, tuhakikishe kwamba tunaipitisha bajeti yetu, bajeti ambayo imezungumza suala zima la uajiri wa polisi, vijana hawa wa polisi, ili tuweze kuajiri. Tukikwamisha hii maana yake tutakuwa hatuna namna ya kufanya. Nakushukuru.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nina maswali mawili ya nyongeza, swali la kwanza; kwa kuwa katika majibu yake ya msingi ameeleza wazi kwamba, Zimamoto huwa wanahusika sana katika kutuliza moto huo endapo majanga yanatokea. Hata hivyo, sio siri mara nyingi Jeshi hilo likifika linakuta magari hayana maji au wamechelewa sasa swali langu kwa Serikali, imejipangaje kuimarisha Jeshi hilo la Zimamoto ili wawe more efficient? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, mioto hiyo ipo katika maeneo yetu tunayoishi au vijijini au kwenye kata zetu au mitaa yetu, lakini wananchi hao nikiweko mimi hatujapatiwa mafunzo ya kutosha kwenye kuzima mioto mikubwa kama hiyo. Wengi ni waathirika wa maeneo hayo na sitaki kurudi nyuma kukumbusha vilio vya Shauritanga na mashule mengine ambayo sitaki kutaja ikaja kuharibu sifa za shule hizo kupata wanafunzi. Je. Serikali itatoa lini mafunzo na kwa msisitizo kabisa ili watu hawa wapate elimu ya kusaidia kuzima mioto hiyo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nachukua fursa hii kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Shally Raymond, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza ameuliza, je, ni nini sasa Serikali inafanya au hatua ambazo inazichukua katika kuhakikisha kwamba inapunguza haya majanga ya moto ambayo yanajitokeza mara kwa mara? Ziko hatua nyingi ambazo kama Serikali tumezichukua ili kuona namna ambavyo tunapunguza, hatuwezi kuondosha moja kwa moja kwa sababu, mengine yanakuja, lakini tunapunguza. La kwanza, ni kuendelea kutoa elimu ama kuendelea kutoa taaluma kwa jamii, kwa sababu tunaamini jamii ikipata taaluma ama ikishiba taaluma ya kutosha majanga haya yatapungua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine tunaendeleza ukaguzi wa majengo. Yapo majengo lazima tuyakague kwanza, yako majengo ya binafsi, yako majengo ya Serikali na yako majengo mengine. Kwa hiyo, tunakuwa tunafanya ukaguzi wa kwenye majengo ili kuona namna ambavyo tunawaelimisha namna ya kujikinga na haya majanga ya moto. Kikubwa zaidi tunao mpango na tumeshaanza, wa kuongeza visima vya dharura kitaalam tunaviita fire hydrants ili ikitokezea taharuki kama ya moto tuwe tuna maeneo ya kuweza kuchota maji na kuweza kuokoa maisha ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni kwamba Je. taaluma huko vijijini inafikaje? Tunavyo vitu vingi ambavyo tumeviandaa ambavyo vinaendelea kutoa taaluma, tunazo zile fire clubs ambazo ziko huko vijijini kwenye kata kwenye vijiji, kwenye shehia ambazo zinaendeleza kutoa taaluma kwa watu. Pia hivi karibuni nimewahi kusema sana tu, hivi karibuni tulifanya makubaliano na watu wale wa skauti ambao wengi wao ni wanafunzi na wako vijijini huko ambao wanafanya kazi kubwa ya kuendelea kutoa taaluma na kuelimisha jamii namna bora ya kujikinga na haya majanga. Vile vile kuelimisha jamii namna bora ya kutoa taarifa mapema kwa sababu changamoto inakuja kwenye utoaji wa taarifa. Nakushukuru sana.
MHE. MAIMUNA S. MTANDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Naomba kuuliza swali la nyongeza; kwanza nishukuru kwa majibu ya Serikali, lakini nataka kujua namna ambavyo Wizara ya Mambo ya Ndani inashirikiana na Wizara ya TAMISEMI wenye shule kuhakikisha kwamba matukio haya sasa yanakoma kwa sababu, yamekuwa yakisumbua mara kwa mara katika shule zetu hasa za mabweni. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimtoe hofu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tunao ushirikiano wa karibu baina ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi na TAMISEMI na hata hawa watu wa Wizara ya Elimu katika kuhakikisha kwamba tunapunguza idadi kubwa ya majanga ya moto na majanga mengine hasa katika maeneo ya shule na maeneo mengine. Tayari tumeshakuwa tunakaa vikao mbalimbali, tumeshapanga mipango mbalimbali ambayo ni mikakati ya kuhakikisha kwamba tunapunguza haya majanga.

Kwa hiyo, hilo Mheshimiwa asiwe na wasiwasi juhudi zinaendelea kazi inaendelea na tutahakikisha kwamba tunapunguza haya majanga kwa kiasi kikubwa. Nakushukuru.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nimshukuru Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake. Lakini, hata hivyo ningependa kujua kuna mfano gani kwa waganga hao wa ramli chonganishi na manabii wa uongo hatua ambazo wamechukuliwa baada ya kupatikana na kadhia hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, je, Serikali haioni sasa wakati umefika wa wale manabii ambao wanadai wanao uwezo wa kuwafufua waliokufa ili kukaa nao kwa karibu ili kuweza kuwafufua wapendwa wetu. Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza je ni mfano gani wowote ambao uliowahi kuchukuliwa hatua wa hawa waganga matapeli na Manabii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama Mheshimiwa Khalifa atarejea kwenye jibu langu la msingi ni kwamba mpaka kufika kipindi cha mwaka 2020 jumla ya kesi 57 za waganga chonganishi na wengine tayari zimesharipotiwa kwasababu ili kesi iwe kesi kwanza iwe reported. Kwa hiyo, kikubwa nimwambie kwamba zipo kesi ambazo zimeshafika kwenye ofisi yetu au zimeshafika Mahakamani, tayari zimo katika mchakato wa kuchukuliwa hatua kwa mujibu wa taratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine nimwambie kwamba hili jambo ni jambo amablo linahitaji utulivu wa kukaa tukafanya utafiti na takwimu za kutosha ili tukilileta hapa tuliseme kwa mujibu wa uhalisia lilivyo. Kikubwa ni kwamba zipo kesi ambazo zimeshakuwa reported. Kuna kesi ilijitokeza Mkoa wa Njombe, yupo kijana aliambiwa na babu yake ili uwe Tajiri na huo utajiri tupate mimi na wewe basi lazima uwe unawaua watoto mpaka wafike idadi fulani. Mwisho wa siku ile kesi ikaripotiwa na tukamshtaki huyo mtu kwa kosa la mauaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna kesi imejitokeza Misungwi huko ya mtu mmoja aliambiwa na mganga hivyo hivyo tapeli ili mimi na wewe tuwe matajiri hakikisha unawaua wanawake halafu unatembea nao. Lengo na madhumuni tuwe matajiri. Hii kesi imeletwa na tumeichukulia hatua kwa hivyo. Kikubwa niseme kwamba hizi kesi zipo kwa zile ambazo zimeripotiwa na hatua za kisheria kwa mujibu wa taratibu zinachukuliwa na majibu yatapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali jingine lilikuwa linauliza je, hakuna haja ya kukaa sasa na hawa wafufuaji ili tuweze kuwafufua wapendwa wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, imani ya kibinadamu inaamini na ndivyo ilivyo kwamba mwenye uwezo wa kuondosha na kurejesha, yaani kufanya mtu akaondoka, akafa ni Mwenyezi Mungu peke yake. Ndiyo maana ilifika wakati tukawa tunasema kwamba kama kutakuwa kuna watu wa namna hii kama alivyoshauri Mheshimiwa Mbunge, tuko tayari kukaa nao tuwaeleweshe, tuwafahamishe ili wafike wakati wasije wakazua migogoro katika jamii. Kwasababu anaweza akatokezea mtu akasema mimi nina uwezo wa kufufua, akachukua pesa za watu. Mwisho mtu akazikwa akafa akasahauliwa. Mwisho wa siku migogoro katika jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa nimwambie tuko tayari kukaa na hao watu ili tujue namna ya kuwaelimisha kuwaeleza kwamba mwenye uwezo wa kufufua na kuondosha mtu kwa maana ya kufa ni Mwenyezi Mungu Subhana Wataalah. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. JANETH E. MAHAWANGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Pamoja na majibu hayo, nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa usalama ni jambo muhimu sana kwenye jamii yetu, je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia magofu ambayo yamejengwa na wananchi hususan maeneo ya pembezoni mwa miji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kutokana na changamoto ya kiusalama hasa maeneo ya pembezoni mwa miji je, Serikali imeandaa utaratibu gani au ina mpango gani wa kupeleka magari ya doria hasa nyakati za usiku kwenye maeneo ambayo hayana vituo vya polisi. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, je, Serikali ina mpango gani wa kumaliza sasa maboma?

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa kazi kubwa ya Serikali ni kuhakikisha kwamba inawapelekea wananchi huduma ya ulinzi na usalama karibu ya maeneo yao. Hiyo ni sehemu ya wajibu kabisa. Lakini na wananchi nao wanafika wakati wanakuwa wanao wajibu kwa kushirikiana na viongozi mbalimbali kusaidia sasa kuona namna ambavyo nao wanajisaidia kujikaribishia hizo huduma kwa kushirikiana na Serikali. Kikubwa tu nimtoe wasiwasi Mheshimiwa Mbunge. Tutajitahidi katika bajeti ijayo tutakapopanga mipango yetu basi tutajitahidi katika maeneo haya ya pembezoni hasa katika mkoa huu basi baadhi ya maeneo hayo tuyape kipaumbele ili tuone namna bora ambayo wananchi wanaweza wakafikishiwa hizo huduma kama ambavyo maeneo mengine yanafika.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini je, kutokana na changamoto hii Serikali sasa ina mpango gani katika kupeleka magari haya kwa ajili ya kufanya doria. Mpango upo, kama ambavyo tumefanya katika mikoa na wilaya na vituo vingine na maeneo mengine na hapa katika maeneo hayo ambayo Mheshimiwa ameyakusudia au ameyataja tunao mpango wa kupeleka magari hayo kufanya doria ili sasa wananchi na wao waweze kupata huduma hizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa ambacho tumekifanya huko, tayari tuna mfumo au tuna utaratibu wa ulinzi shirikishi ambao askari polisi/Jeshi la Polisi wanashirikiana na raia/ jamii katika kuhakikisha kwamba maeneo ya wananchi yanapata huduma ya ulinzi kama maeneo mengine. Kikubwa nimwambie Mheshimiwa asiwe na wasiwasi, atulie awe na Subira. Mambo mazuri yanakuja maana kazi inaendelea.
MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kuniona. Wilaya ya Ngara ina changamoto ya uhaba wa askari na Wilaya hii inapakana na nchi jirani za Rwanda na Burundi. Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka askari wakutosha ili wananchi waweze kulindwa na mali zao? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, je, tuna mpango gani sasa wa kupeleka askari ama ulinzi katika maeneo ambayo ameyataja.

Mheshimiwa Naibu Spika, narejea tena kusema kwamba wajibu na jukumu la Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kupitia Jeshi la Polisi ni kuhakikisha kwamba maeneo yote yanapata huduma ya ulinzi na usalama ili wananchi waishi kwa amani. Ikiwa pana watu wageni, ndani ya Tanzania hii lakini wajibu wetu ni kupeleka. Nimtoe hofu, asiwe na wasiwasi, maeneo hayo kwa kuwa amehisi kwamba yana upungufu wa ulinzi, tunayachukua na tunapeleka ulinzi ili wananchi na wao waweze kuishi kwa amani na wapate huduma za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuongeza maswali mawili ya ziada. Swali langu la kwanza, nataka nijue kwa kuwa, suala la ubakaji na ulawiti na unyanyasaji kwa watoto haliko Tanzania pekee, lipo katika nchi mbalimbali. Nilitaka kujua Serikali inashirikiana na mashirika gani, ili kuhakikisha suala hili linakomeshwa?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili, kwa kuwa, kuna maafisa wa madawati katika maeneo kadhaa, ili kusaidia kupambana na masuala ya ulawiti, ubakaji na unyanyasaji kwa watoto, nilitaka kujua wanawawezeshaje maafisa wale, ili waepukane na rushwa, lakini pia waweze kufanya kazi zao kwa ufanisi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, anataka kujua ni mashirika gani ya kimataifa au mashirika gani ambayo tunashirikiananayo katika kupambana na jambo hili. Kwa kweli, niseme tu kwamba, yapo mashirika mengi ambayo tunashirikiananayo. Yapo ya ndani na nje ya nchi ambayo tunashirikiananayo katika kupambana dhidi ya matukio haya ya uhalifu, hasa ya udalilishaji wa kijinsia. Kwa upande wan je huko tuna mashirika kwa mfano ya UNICEF, kuna shirika La WHO (World Health Organization), tuna UN Women, tuna USAID, tuna Save the Children, hapa tuna akina taasisi zile zinazoshughulikia masuala ya kisheria. Kwa hiyo, kwa ufupi tuna taasisi nyingi ambazo tunashirikiana nazo katika kuhakikisha kwamba, tunapambana dhidi ya haya matukio ya udhalilishaji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu vipi tunawawezesha hawa maafisa wa madawati; maafisa wa madawati tuna mambo mengi. La kwanza tuna mfumo maalum ambao upo kwa ajili ya uwezeshaji na ufuatiliaji wa matukio ya udhalilishaji, lakini pia tumekuwa tunawapa elimu ya kisheria, tunawapa elimu ya protections, tunawapa elimu ya kijamii. Elimu ambazo zinawasaidia wao kuweza kuchukua hatua pale tukio linapotokea, lakini zaidi tumeanzisha kwenye vituo pamoja na kwamba sio vyote, lakini vipo vituo ambavyo tumewawekea usafiri ambao huwa wanatumia kwa ajili ya kufuatilia hayo matukio mara tu yanapotokea. Nakushukuru.
MHE. BALOZI DKT. PINDI H. CHANA: Mheshimiwa Spika, asante. Kwa niaba ya wananchi wa Mkoa wa Njombe, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; Serikali imesema kwamba, wanatafuta hizi fedha shilingi milioni 322. Ningependa kujua mkakati mzima wa upatikanaji wa hizi fedha na zitakuwepo kwenye bajeti ipi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; eneo ambalo wamepanga kujenga Ofisi ya Mkoa wa Njombe (Central Police), ni eneo hilohilo Ofisi ya Mkoa imepangwa kujengwa na Mahakama ya Mkoa; Ofisi ya Mkoa na Mahakama zimeshajengwa, sasa hii bado.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Njombe wangependa kujua ni lini hasa ofisi hii itajengwa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Balozi Dkt. Pindi Hazara Chana, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Njombe, maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza Mheshimiwa anauliza; je, katika bajeti hii tumepanga kuweza kupata hizo fedha?

Mheshimiwa Spika, kubwa tu nimwambie kwamba katika bajeti hii hakuna fungu hili, lakini tutajitahidi katika bajeti ijayo pesa hizi ziwepo na tumuahidi Mheshimiwa kwamba, tutampa kipaumbele katika kuhakikisha kwamba, eneo hili linapata kituo hicho cha polisi ambacho kitatoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, lakini je, ni lini sasa Serikali italipa hiyo fidia? Nimwambie tu kwamba, tutajitahidi na tumuahidi mwaka ujao wa fedha tutajitahidi tulipe hiyo fidia, ili sasa ujenzi huu uweze kuanza haraka na wananchi waweze kupata huduma hizo za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Spika, ahsante na nashukuru kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali langu ni je, Serikali inatumia utaratibu gani wa kulipa madeni ya askari ambao unaendelea kwa kuwa wameanza kulipa 2018/2019 na wameacha 2017, lakini pia askari waliopandishwa vyeo kutoka Mainspekta kuwa Warakibu wa Polisi 99, askari 99 ambao walipanda mwaka 2013 mpaka 2017 hawajalipwa mshahara kwa cheo hicho wameanza kulipwa 2018? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali hili la Mheshimiwa Jesca kwamba suala hili ni suala ambalo linahitaji takwimu na linahitaji data za uhakika. Kwa hiyo, kubwa tu nimwambie Mheshimiwa kwamba pamoja na kwamba utaratibu umeshaanza kupangwa, lakini nimuombe tu kwamba, suala hili aendelee kulipa muda ili tukalifanyie kazi halafu tutajua namna ya kuja kumjibu, nakushukuru.
MHE. LAZARO J. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri lakini nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza, Serikali inatarajia kupata fedha hizo lini ili wale wananchi waweze kulipwa fidia badala ya kuendelea kusubiri kwa muda mrefu?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kutokana na umbali uliopo kati ya Makao Makuu ya Wilaya na Kituo cha Polisi ambacho kinatumika kama Makao Makuu ya Polisi, Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha za OC ili ofisi ile ya Polisi ya Wilaya iweze kujiendesha bila karaha wala kuombaomba fedha kwa wadau wengine?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nyamoga, Mbunge wa Kilolo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ameuliza, je, lini Serikali italipa fidia? Nataka nimjibu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inao mpango na italipa fidia wananchi hao kwa ajili ya eneo hilo kwa sababu inatambua umuhimu wa uwepo wa Kituo hicho cha Polisi ili wananchi waweze kupata huduma hizo. Kubwa zaidi tayari tumeshatoa maelekezo na wameshafanya tathmini wataalam kutoka Halmshauri ya Wilaya ya Kilolo inayohitajika kwa ajili ya fidia hiyo na tayari tumeshaelekeza pa kwenda kupata fedha hizo kwa ajili ya kulipa fidia wananchi hao. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali inaendelea kufanya juhudi kuona namna bora ya kuwalipa fidia wananchi hao. Kubwa Mheshimiwa Mbunge aendelee kuzungumza na wananchi wake ili waendelee kuwa na subra jambo hilo limo mbioni kushughulikiwa.

Mheshimiwa Spika, swali la pili anauliza kama Serikali ipo tayari kuongeza OC. Niseme tu kwamba Serikali ipo tayari kuongeza OC lakini ni pale ambapo tutakuwa na fedha ya kutosha kufanya hivyo. Kwa hiyo, kwa sasa waendelee kuwa na subra hivyo hivyo tubananebanane lakini tunao mpango huo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na hayo upo mbadala ambao tumeshauchukua, kwanza tumeongeza operesheni ama doria za mara kwa mara katika maeneo ambayo wananchi wako mbali na vituo vya polisi ili waweze kupata hizo huduma za ulinzi. Vilevile tunaendelea kusisitiza ulinzi shirikishi ambapo inasaidia huduma za ulinzi kufika mpaka maeneo ya vijijini kwenye kata. Lengo na madhumuni ni wananchi waendelee kupata huduma za ulinzi na waishi kwa amani.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. OMAR ALI OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa jibu zuri la Mheshimiwa Naibu Waziri, pamoja na hayo nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba posho ya shilingi 100,000 ambayo ilikuwa inatolewa kwa ajili ya kuwawezesha askari wetu waweze kukidhi haja ya kuweza kujenga, tukiangalia kwa mtazamo ni kwamba posho hiyo ilikuwa ni ndogo na hata askari wakipewa miaka 100 hawawezi kufanya ujenzi kwa posho hiyo.

Je, Serikali ina utaratibu gani wa kuwawezesha askari wetu kuwaongezea posho hii ili iendane na utaratibu wa kuweza kujenga kwa askari wetu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba mbili; je, sasa Serikali haioni kwamba kuna haja kwa Wizara kuhakikisha kuona kwamba pamoja na kwamba askari wetu wanaintelijensia ya hali ya juu, hatuoni sasa kwamba kuna haja sasa ya ule utaratibu wa mwanzo kuweza kutumika ili kwamba askari wetu tuweze kuwaweke katika mazingira mazuri waweze kulinda nchi hii, raia pamoja na mali zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi naomba sasa kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omar Ali Omar kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, je, Serikali ipo tayari ama ina utaratibu gani sasa wa kuongeza hii posho?

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunayo dhamira kwa sababu kwanza nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba vyombo vyetu vya ulinzi hasa Jeshi la Polisi wanafanya kazi nzuri na kwa kweli tunayo kila sababu ya kuwatengenezea mazingira mazuri ya kuendelea kufanya kazi vizuri, katika hili tunawapongeza sana. Kikubwa ni kwamba utaratibu wa kuongeza hizi posho upo, tumeshaupanga/tumeshaufikiria maana hata katika bajeti ambayo tuliiwasilisha juzi tulilizungumza hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa awe na stahamala kwa sababu hii mipango inahitaji fedha na tupo mbioni kuhakikisha kwamba tunatafuta hizo fedha ili tuweze kuwaongezea kwa sababu hatuwezi tukasema kwamba kesho tutawaongezea, kwa hiyo, kesho watazipata lakini the way ambavyo kasungura ketu kananenepa ndivyo ambavyo tutakapokuwa tunawaongezea na wao hii posho ili sasa waendelee kufanya kazi nzuri zaidi ya kulinda raia na mali zao. Kwa hiyo, hiyo nia ya kuwaongezea posho ipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini je, hakuna haja ya kurejesha ule utaratibu wa mwanzo, mimi nadhani Mheshimiwa Mbunge atupe nafasi tuende tukakae na wenzetu tukalifikirie hili, tukapange halafu tutaona sasa namna bora ya kuboresha haya mambo ili sasa kuweza kurejesha ule utaratibu wa mwanzo ambao kama yeye Mheshimiwa Mbunge ameuzungumzia. Nakushukuru. (Makofi)

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na majibu mazuri ya Naibu Waziri Khamis, lakini nataka nikubaliane na muuliza swali la msingi Mheshimiwa Lambert pamoja na maswali yake ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ni kweli tunakubaliana kwamba vijana hawa askari polisi wanafanya kazi nzuri kwa nchi na Taifa lao na pengine wanafanya hivyo katika mazingira magumu na wengine kulingana na vyeo vyao ni vigumu sana kujikomboa na kupata hata maisha mazuri baada ya kumaliza utumishi wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lililosemwa katika swali la msingi ni kama je, Serikali haioni haja ya kuwapatia vijana hawa viwanja kwa bei nafuu? Nataka niseme sisi kama Wizara tunalichukua hili, tutajadiliana na wenzetu wa Wizara ya Ardhi tuone uwezekano huo kwa sababu ni jambo jema kabisa na wengine kweli wanamaliza/wanastaafu wakiwa kwanza na umri mdogo kulingana na Kariba ya ajira yenyewe ya Jeshi la Polisi, mtu ana miaka 54 anastaafu, halafu hana hata nyumba wala kiwanja. Nataka nikubaliane kwamba acha tulifanyie kazi, tuone kwa mfumo ambao uliopo kama tunaweza tukawapatia vijana hawa angalau viwanja, angalau kwa wale wa vyeo fulani fulani ambao unajua wapo kidogo underprivileged. Nakushukuru sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Waziri, mmezungumzia upande wa viwanja nafikiri pia Serikali mtajipanga na hoja ya pili ya muuliza swali ameuliza mambo mawili; msamaha wa kodi katika vifaa vya ujenzi pamoja na viwanja kwa bei elekezi. Kwa hiyo, nafikiri…, karibu.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, huko nyuma tulikuwa na utaratibu wa duty free shops kwa ajili ya hawa askari. Maduka haya yalitumika na ukatokea ukiukwaji mkubwa sana wa taratibu za kikodi na kutokana na mazingira hayo mambo mengi mabaya yalitokea, Serikali ikaona bora kuondoa ile kwa sababu waliokuwa wananufaika ni watu fulani, fulani tu hata walengwa pengine walikuwa hawanufaiki, tukaona bora waingiziwe fedha zao na kwa utaratibu wa sasa wanalipwa shilingi 300,000 kila baada ya miezi mitatu, ni kitu fulani kuliko wengine ambao walikuwa vijijini huko hata duty free shops hizo hawazioni. Na utaratibu huo wa ku-institutionalize leo ni vigumu sana. Kwa hiyo, utaratibu wa fedha kuingizwa kwenye akaunti zao umekuwa ni bora na wanaufurahia sana. (Makofi)
MHE. RASHID ABDALLA RASHID: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimshukuru Naibu Waziri kwa majibu mazuri, lakini nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza kwa kuwa eneo tayari lipo na kwa kuwa nafahamu kwamba kuna matofali ya kutosha katika Kambi ya Mfikiwa yaliyobaki kwa ajii ya ujenzi wa nyumba za Polisi Mfikiwa na mimi nikiwa mdau wa upatikanaji wa matofali hayo.

Je, ni lini Wizara itatupatia matofali hayo ili kwa kushirikiana na wananchi wangu wa Jimbo la Kiwani tuweze kuanza ujenzi wa kituo hicho?

Swali la pili, wananchi wa Shehia ya Kendwa kwa kushauriwa na Jeshi la Polisi Mkoa wa Kusini Pemba walitakiwa waanzishe Jengo kwa ajili ya polisi jamii na wananchi hao kwa kutii walianzisha jengo hilo ambapo sasa lina miaka nane.

Je, ni lini Wizara italimaliza jengo hilo ili wananchi waweze kupata huduma?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Rashid Abdalla, Mbunge wa Jimbo la Kiwani kutoka Kusini Pemba.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza linazungumzia kuhusu matofali; ni kweli katika eneo lile la Mfikiwa yapo matofali na matofali yale jumla yake ni 32,000 na matofali yale yaliletwa pale kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za askari makazi ya askari pale Mfikiwa na siyo matofali tu, lakini yapo na mabati ipo na rangi. Lakini kwa bahati nzuri au bahati mbaya ikafika wakati kidogo tukapungukiwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kuendeleza ujenzi huu.

Kwa hiyo, matofali haya nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba hayapo tu kwamba maana yake kazi imekwisha, kazi ya ujenzi wa nyumba zile azma ya Serikali iko pale pale, kwa hiyo, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba aendelee kustahimili tupo mbioni tutahakikisha kwamba kwa kushirikiana yeye na wadau wengine werevu tupate matofali na vifaa vingine vya kutosha ili tukajenge Kituo cha Polisi hapo Kiwani.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo nimwambie tu kwamba azma ya Serikali ni kuendeleza kujenga nyumba hizi na nyumba hizi zipo katika hali ya kujengwa kwa sababu tayari ipo nyumba moja imeshaanza kujengwa na imeshafikia katika hatua ya lenta.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, je, ni lini sasa Serikali itamaliza boma lile la polisi jamii. Kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Mbunge kwa kazi kubwa na nzuri ambayo anaifanya katika Jimbo la Kiwani, kwa sababu amekuwa ni mdau mzuri ambaye anatusaidia Serikali hasa katika masuala ya ulinzi na usalama, hiki kituo ambacho kinazungumzwa cha polisi jamii amesaidia kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba anasaidia wananchi kuweza kupata huduma hizi. Kwa hiyo kikubwa nimwambie tu kwamba tutajitahidi katika mwaka ujao wa fedha tuweke hilo fungu kwa ajili ya kumsaidia kumalizia hili boma ama hiki kituo ambacho kimeshaanza cha askari jamii katika Shehia hii ya Kendwa. Nakushukuru.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Naibu Waziri nilikuwa naangalia kwenye jibu la msingi linaonesha kwamba huko Kiwani mpaka sasa hivi hakuna eneo lililotengwa; wakati huo huo kuna mahali kuna matofali yamewekwa na ujenzi umefika mahali. Sasa hebu fafanua kidogo, haya matofali yako wapi ili nijue swali la nyongeza la Mbunge linaendana na hili jibu la msingi au hapana?

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, swali aliloliuliza kwamba kule Kusini Pemba kuna eneo la tuseme ni Kambi ya Askari Polisi panaitwa Mfikiwa, pale Mfikiwa Serikali kupitia Jeshi la Polisi iliamua ijenge nyumba za makazi ya askari polisi yaani Mfikiwa na huko Jimboni kwake ni mbali kidogo.

Kwa hiyo, kilichokuja kuamuliwa kwamba kuna matofali yale yeye ameona kwamba yako kwa muda mrefu yamekaa, kwa hiyo, anaona kwanini Serikali yale matofali yasichukuliwe yakapelekwa Kiwani ili wananchi wa Shehia za Jombwe, Kendwa, Muwambe, Mchake, Mtangani, Kiwani wajengewe kituo kile cha polisi sasa yale matofali azma ya Serikali ilikuwa ni kujenga nyumba za askari na kila kitu kipo tulipungukiwa kidogo na fedha ndicho ambacho anataka apelekewe yale matofali tukamwambia kwamba tutamfanyia maarifa tumpelekee matofali mengine.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kituo cha polisi cha Itaka ambacho kinahudumia kata zaidi ya tano ikiwepo kata ya Nambizo pamoja na Halungu kinakabiliwa na changamoto kubwa sana kwanza jengo lake limechakaa, lakini pili hakuna pia vitendea kazi lakini kama haitoshi kituo kile cha polisi kina polisi wanne tu. Naomba kufahamu Serikali imejipanga vipi katika kukabiliana na hiyo changamoto? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juliana Shonza kama ifuatavyo; Serikali tunafahamu na tunatambua changamoto iliyoko katika Jeshi la Polisi na tunafahamu kwamba bado kuna vituo vimechakaa, tunafahamu kwamba tuna changamoto ya vitendea kazi, lakini pia tunafahamu kwamba tuna baadhi ya upungufu wa watumishi katika Jeshi. Kikubwa nimwambie Mheshimiwa aendelee kutustahimilia kwa sababu hatua za kuhakikisha kwamba tunachanganua ama tunatatua hii changamoto ama hizi changamoto tumeshazianza zikiwemo za uajiri, za upatikanaji wa vitendea kazi na za kurekebisha majengo yaliyochakaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo kubwa nimuombe tu Mheshimiwa aendelee kustahimili sisi kama Serikali kama Wizara tupo mbioni kuhakikisha kwamba watengenezea mazingira mazuri wananchi kwa ajili ya kupata huduma nzuri za ulinzi na usalama.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana; kama ilivyo vituo vingi vya polisi vilivyochakaa, Kituo cha Matangatuwani kilichoko katika Jimbo la Konde Wilaya ya Micheweni Mkoa wa Kaskazini Pemba kimechakaa na kwa kweli ni kibovu, ikinyesha mvua ni bora ukae chini ya mwembe utapata stara kuliko Kituo cha Matangatuwani.

Je, ni lini Serikali itakifanyia ukarabati mkubwa kituo hiki cha Matangotuwani?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Khalifa Mohamed kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Khalifa amekuwa ni mdau wetu muhimu wa kutusaidia kwanza kutuonesha maeneo ambayo tunatakiwa sisi kama Serikali tuyafanyie marekebisho, lakini pia amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba anatoa hata kilicho mfukoni kwake au katika Mfuko wa Jimbo kuhakikisha kwamba anawasaidia wananchi katika kupata huduma za ulinzi na usalama, hili nimpongeze sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kikubwa nimwambie kwamba nirejee tena kwamba bado tunatambua kwamba kuna baadhi ya changamoto ambayo sisi ni sehemu ya wajibu wetu kuhakikisha kwamba tunazitatua ili kuhakikisha kwamba wananchi wetu wanapata huduma nzuri za kiulinzi na usalama. Kituo ambacho anakizungumza ni kweli kipo na mimi binafsi nimefika na hali nimeiona, lakini kikubwa nimwambie hata kama akinifaa kwenye bajeti ambayo tumeiwasilisha tumeisoma hivi karibuni tumezungumzia namna ambavyo tunaenda kurekebisha vituo vya polisi na nyumba na baadhi ya huduma nyingine ili sasa wananchi waweze kupata huduma bora za kiulinzi na usalama. Nimwambie tu kwamba na yeye ni miongoni mwa vituo ambavyo tutajitahidi turekebishe ili tuone namna ambavyo na wao wanapata huduma nzuri. Nakushukuru.
MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi; Kituo cha Polisi Nanyamba kilijengwa huko nyuma kwa ajili ya kuhudumia Tarafa ya Nanyamba lakini sasa hivi Halmashauri ya Mji wa Nanyamba ni Makao Makuu ya Halmashauri hiyo mpya na kuna ongezeko la watu na kituo hicho kimechoka na keshokutwa nitakabidhi bati 70 kwa ajili ya kukarabati.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuunga jitihada zetu kufanya ukarabati mkubwa wa kujenga Kituo kipya cha Polisi Nanyamba?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba sasa nijibu swali la Mheshimiwa Chikota kama ifuatavyo:-

Kwanza nimpongeze sana kwa juhudi ambazo anazifanya za kutusaidia na ninajua anafanya haya kwa sababu aliwaahidi wananchi kwamba atawatumikia na atawasaidia kuhakikisha kwamba wanapata huduma bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, azma ya kutoa mabati na vingine ambavyo utahakikisha kwamba wananchi wanahitaji aendelee kufanya hivyo na sisi tuko pamoja na yeye.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu kwamba zipo jitihada ambazo sisi kama Serikali kama Jeshi la Polisi tuna mpango wa kufanya si kituo hiki tu cha alichokitaja, lakini na vituo vingine. Kwa hiyo, kikubwa tumwambie kwamba tutaangalia na bajeti itakavyoturuhusu, lakini tumwahidi kwamba moja ya miongoni mwa maeneo ambayo tutayapa kipaumbele kuhakikisha kwamba wananchi wanapata kituo bora na kukifanyia marekebisho ni katika kituo chake cha Nanyamba. Nakushukuru.
MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; ili askari wangu pale Iringa wapate utulivu na kuimarisha ndoa zao na familia wanahitaji makazi bora. Je, ni lini Serikali sasa itatujengea makazi bora ya askari katika Kituo Kikuu cha Polisi Iringa?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jesca Msambatavangu, Mbunge wa Iringa Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze sana na yeye kwa juhudi kubwa ambayo anatusaidia katika kuhakikisha kwamba anawasaidia wananchi, lakini kikubwa nimuahidi kwamba katika mwaka wa fedha ujao tutajitahidi na tutahakikisha kwamba hili eneo ambalo yeye amelizungumza tulipe kipaumbele ili tu wananchi wa eneo hilo waweze kupata na wao huduma za ulinzi na usalama bila ya tatizo lolote, nakushukuru.
MHE. MARTHA F. MARIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, miongoni mwa vigezo vinavyowakwamisha vijana wetu wa Kitanzania hususan waliopo katika mikoa inayopakana na nchi jirani ikiwemo Mikoa ya Katavi, Kigoma na mingineyo ni pamoja na ucheleweshwaji na upatikanaji wa namba za NIDA.

Je, Serikali haioni sasa kuna umuhimu wa kutokutumia kigezo hiki wakati vijana wanapokuwa wanatumia ajira ili kuwawezesha vijana wetu waweze kupata ajira kwa kuwa mchakato huo bado haujakamilika?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali langu la pili; ni kwanini sasa mfumo wa NIDA usiunganishwe na mfumo wa RITA wa vyeti vya kuzaliwa ili kuwawezesha Watanzania pale tu mtoto anapozaliwa aweze kupata cheti kimoja kinachounganisha kuonyesha kwamba huyu ni raia kwa kuzaliwa? Ahsante sana.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Martha Festo Mariki, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa kwa kuwa umefika wakati ameona umuhimu wa wananchi hasa wa mkoa wake kufanyiwa haraka katika kupata vitambulisho huku akiwa anajua kwamba vitambulisho kwa sasa NIDA ndiyo kila kitu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini naomba sasa nianze kujibu swali la kwanza, kwamba, je, Serikali sasa haioni haja ya kuondosha hiki kigezo cha NIDA ili sasa mambo mengine yaweze kuenda yakiwemo ya vijana kuweza kupata ajira?

Mheshimiwa Naibu Spika, ukweli ni kwamba tumeamua kuweka kigezo hiki ili kuweza kuwajua ni nani wenye sifa na nani wasiokuwa na sifa; na tumeamua kukiweka kigezo hiki ili kuona kwamba nani ambao wana Utanzania na nani ambao hawana Utanzania. Sasa kwa kusema moja kwa moja kigezo hiki kukitoa basi ni jambo ambalo linahitaji procedure, twende tukakae na watu wa utumishi na taasisi nyingine. Nimwambie tu Mheshimiwa kwamba jambo hili tunalichukua na tutakwenda kuona namna ya kulifikiria.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kikubwa kingine ninachotaka niseme ni kwamba, na hapa nataka nitoe agizo lakini pia nitoe wito kwa mamlaka hii inayosimamia; kwamba kwa sasa tuone namna ya kuwapa zaidi kipaumbele vijana ambao wanakwenda kutafuta ajira ili waweze kupatiwa hivi vitambulisho kwasababu tumeona na tumegundua kwamba kweli hii imekuwa ni changamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pamoja na yote hayo nichukue fursa hii niwaambie Waheshimiwa Wabunge kwamba bado kuna wilaya vitambulisho vipo wenyewe hawajaenda kuvichukua, sasa matokeo yake tunaendelea kupata lawama. Tunataka tutoe wito tuwaambie Waheshimiwa Wabunge kwa kushirikiana na viongozi wengine huko wa Chama na Serikali muwaambie watu waende wakachukue vitambulisho vyao. Yapo maeneo vitambulisho vipo lakini hawajaenda kuvichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwamba, kwanini sasa tusiunganishe RITA na NIDA. Lengo na azma ya Serikali siku zote ni kuhakikisha kwamba wanatengeneza muunganiko wa mfumo ili wananchi waweze kupata huduma kwa urahisi zaidi. Sasa kuunganisha RITA na NIDA si tatizo, Serikali ipo tayari kuunganisha mifumo lakini kuziunganisha taasisi nadhani ni jambo ambalo tunahitaji tukae sasa tufikirie tuone namna bora ya kuziunganisha hizi. Ni kweli zote ni taasisi za Serikali lakini zinao utofauti katika muundo na katika majukumu yake. Kwa hiyo nalo hili pia tutalichukua tuone namna ambavyo tunaweza tukaenda tukasaidia wananchi. Nakushukuru.
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ili niulize maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa ajali inapotokea wamiliki wa vyombo vya moto hupewa mara moja bima yao wanapokwenda kudai chombo kama imeharibika, lakini hawa waathirika ambao ni abiria wanaopata ajali wamepoteza maisha au viungo wamekuwa wakisumbuliwa sana na hawa bima.

Je, nini kauli ya Serikali kutokana na usumbufu mkubwa sana wanaopata abiria wanaopata ajali barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa abiria wengi sana wanaotumia vyombo vya moto wanapopata ajali wanakuwa hawana uelewa wa kutosha na mara nyingi sana sasa hivi tumetumia electronic ticketing yaani kule nyuma hakuna elimu yoyote.

Je, sasa Serikali haioni ni wakati sasa wa kuhakikisha kwamba katika vituo vya kusubiria abiria kuwepo na mabango na matangazo ili kutoa elimu ya kutosha kwa abiria wanapopata ajali nini wafanye? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ritta Kabati, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Iringa.

Kwanza nataka nichukue fursa hii nimpongeze sana kwa kazi nzuri ambayo anaifanya katika Mkoa wake. Mheshimiwa Ritta amefika hatua ya kukarabati Kituo cha Polisi na ujenzi wa kumalizia Kituo cha Polisi katika Kata ya Semtema. Hakika amefanya kazi kubwa, kwa hili nampongeza sana lakini na wengine pia watusaidie kufanya hiki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niombe kujibu maswali mawili. Inapotokea ajali ni kweli mmiliki wa chombo anapata fidia kama amejiunga ama amejihusisha na bima, lakini je vipi kuhusu sasa hawa abiria. Ni kweli hii ni changamoto na bado kuna changamoto nyingine kwa upande wa wananchi. Hapo nataka niwaambie kitu kwamba changamoto ya kwanza wanapopata ajali wanakuwa hawajui namna bora ya uandishi wa barua za kuombea zile fidia zao, kitu ambacho mwisho wa siku kinakuja kuwafanya wao aidha kuchelewa au kukosa kabisa kuweza kupata zile fidia kutoka bima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingine kwa kweli ipo kwenye upelelezi kwamba wale watu wa bima hawawezi kutoa zile fedha za fidia unless mpaka wahakikishe kwamba wamepata attachment ya upelelezi kutoka Jeshi la Polisi. Kwa hiyo, hapo nataka nitoe wito pia kwa Jeshi la Polisi kwamba wahakikishe wanafanya haraka kupeleka ripoti za upelelezi kwa hawa wananchi ambao wanapata ajali ili sasa waweze kupata fidia zao kwa haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kikubwa zaidi uelewa mdogo wa hii taaluma ya bima. Hapa natala nitoe agizo kwa Jeshi la Polisi, kwamba pamoja na kazi nzuri ya utoaji wa elimu kwa wananchi juu ya namna bora ya utumiaji wa barabara, lakini suala la elimu hii ya bima ya kuweza kupata mafao iendelee na kazi ifanyike vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine alikuwa anauliza je, sasa tuna mpango gani wa kuweka haya mabango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mabango yapo, kazi imeanza na inaendelea, lakini kingine tunaendeleza taaluma ambazo kupitia mabango, vyombo vya habari, vijiwe vya bodaboda, shule pamoja na kupitia kila mahala; tunawaelewesha watu namna bora ya kutumia barabara na kuepuka na ajali. Kikubwa zaidi tumeshaweka ishara na alama za barabarani ambazo pia zinasaidia watu kuweza kujua namna ya kuepuka hizi ajali za barabarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. MOHAMED SULEIMAN OMAR: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Kwanza nashukuru majibu ya Serikali kwa kufuatia maswali yangu haya; lakini swali langu la kwanza katika maswali yangu ya nyongeza kwamba kama kwa mujibu wa majibu aliyonipa Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba inakiri kwamba Mamlaka ya kule Zanzibar pia inayo sheria yake ambayo inatambua hizi sheria za faini za papo kwa papo; je, ni kwa nini Jeshi la Polisi sasa limeshindwa kusimamia sheria hizi za papo kwa papo pale barabarani kwa kutumia hizi mashine za EFD? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwamba ni lini sasa Wizara ya Mambo ya Ndani itakaa na mamlaka husika za kule Zanzibar ili kuona Jeshi la Polisi zinaanza kutumia mashine hizi na ukizingatia kwamba itapunguza malalamiko ya wananchi na itapunguza masuala ya rushwa lakini pia itapunguza zile ajali ambazo zitaweza kuepukika? Nashukuru sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI: Mheshimiwa Spika, naomba ama napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Malindi Mheshimiwa Mohamed Suleiman Omar maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, je, kwa nini Jeshi la polisi limeshindwa? Jeshi la polisi halijashindwa kusimamia taratibu, kanuni na sheria za usalama barabarani katika hili suala la kutumia mashine hizi hapa kuja jambo kidogo, Zanzibar kuna mamlaka inaitwa Mamlaka ya Usafirishaji au Mamlaka ya Usalama Barabarani ambayo ina sheria yake sheria namba saba na Bara kuna Baraza la Taifa la kusimamia usalama barabarani ambalo nalo lina sheria yake kama tulivyoeleza, lakini kama hilo halitoshi mamlaka hivi zote zina utaratibu wake na kanuni zake ambazo zinasimamia pamoja na kwamba Jeshi la Polisi ndio muhimili mkubwa ambao unasimamia mamlaka hizi.

Kwa hiyo, haijashindwa kusimamia tatizo lililokuwepo ni changamoto ya sheria kwamba hawa wanasheria yao, wana kanuni yao, hawa wana mamlaka yao pamoja na kwamba Jeshi la polisi ndio hilo. Kwa hiyo jeshi la polisi halijashindwa kusimamia sheria hii.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; je, ni lini sasa Serikali hasa kule Zanzibar itaruhusu matumizi ya hizi mashine? Nimwambie tu kwamba kwa kuwa sheria ipo na mamlaka inayosimamia usalama barabarani ipo na sheria yake ipo kikubwa ni kwamba sasa hivi tupo katika harakati za kukamilisha kanuni itakayokuja kusimamia sheria hizi ili sasa hii sheria ya kutumia hizo mashine kwa ajili ya kukinga hizo ajali na mambo mengine zianze kutumika.

Mheshimiwa Spika, kubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge awe na subira kidogo sana ili tumalize hizo kanuni na sheria zianze kutumika kote kote.
MHE. KASSIM HASSAN HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Swali la kwanza, kituo hiki kina miaka 13 hakijamalizika, je, Waziri atakuwa tayari kuongozana nami kwenda kuzungumza na wananchi wa Jimbo la Mwanakwerekwe?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali la pili, kwa kuwa uhalifu umeongezeka katika Jimbo la Mwanakwerekwe, sasa hivi kuna vibaka na waporaji wengi lakini hata miundombinu ya Serikali nayo imekuwa ikiharibiwa kwa makusudi.

Je, Serikali inatoa tamko gani kuhusiana na kadhia hii wanayoipata wananchi wa Jimbo la Mwanakwerekwe?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kassim Hassan Haji, Mbunge wa wananchi wa Jimbo la Mwanakwerekwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu rafiki yangu Mheshimiwa Kassim niko tayari kuambatana naye kwenda katika kituo kile na kukiona. Nimuambie kwamba kituo kile nakifahamu na kipo kwa muda mrefu ni kweli, lakini niko tayari kuambatana naye kwenda kukiangalia kituo kile na kuona namna ambavyo tunaweza tukawasaidia wananchi ili kuimarishiwa hizi huduma za ulinzi na usalaama katika eneo lao.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini swali lingine ni kuhusu vitendo hivi vya uhalifu ambapo vijana wanafanya vitendo vikiwemo vya uvunjifu wa miundombinu na uharibifu wa vitu vingine. Ndani ya jimbo lake kuna kituo kingine kikubwa cha Mwanakwerekwe na hicho kinafanya kazi muda wote, hasa kupitia kituo hiki tutajitahidi tuwe tunafanya doria za mara kwa mara ili kuweza kuwakamata na kuwashughulikia wale wote ambao wanavunja amani ama wanafanya vitendo vya uhalifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini lingine tuko tayari kuendeleza na kuimarisha ulinzi shirikishi ili wananchi na wao waweze kutoa mchango wao katika kulinda amani ya wengine. Kikubwa, tuko tayari kuwachukulia hatua za kisheria na kinidhamu wale wote ambao watakuwa wanafanya vitendo hivi. Nakushukuru.
MHE. CONDESTER M. SICHALWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi. Kwa kuwa Wilaya ya Momba makao yake makuu yako ndani ya Halmashauri ya Momba, je, ni lini Serikali itatujengea kituo cha polisi ambacho kina hadhi ya wilaya ili kiweze kusaidia kuepusha changamoto na uovu wote ambao unaoendelea ndani ya Jimbo la Momba? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Condester Sichalwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba lengo la Serikali kupitia Jeshi la Polisi ni kuhakikisha kwamba wananchi wote wanapatiwa huduma za ulinzi na usalama kupitia kila chombo ambacho wananchi watakuwa wanahitaji. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba awe na Subira, tutajitahidi sana tuhakikishe kwamba ndani ya jimbo hilo au ndani ya eneo hilo ambalo limekosa hicho kituo cha polisi basi tuone namna ya kuweza kupata fedha ili tukawatengenezee wananchi kituo cha polisi waweze kupata huduma za ulinzi. Nakushukuru.
MHE. USSI SALUM PONDEZA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii nami nimuulize Mheshimiwa Naibu Waziri swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Jimbo langu la Chumbuni lina matatizo ambayo yanafanana na Jimbo la Mwanakwerekwe ambalo swali la msingi limeulizwa. Nimekuwa nikiuliza kwa miaka mitano kuhusu Kituo chetu cha Chumbuni ambacho kinahudumia karibu wilaya nzima ya pale mjini, shehia zaidi ya sita, tangu kilikuwa kinafunguliwa asubuhi kinafungwa saa kumi na mbili sasa hivi kimefungwa kabisa. Je, ni lini na sisi tutapata kituo cha polisi kwa sababu kinahudumia zaidi ya shehia sita?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ussi Pondeza, Mbunge wa wawanachi wa Jimbo la Chumbuni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuna baadhi ya vituo tulivifunga kwa sababu nyingi sana. Kuna vituo vingine vilifungwa kwa sababu kubwa tulikuwa na upungufu hasa wa rasilimali watu, kwa maana ya polisi. Nimwambie tu Mheshimiwa kwa kuwa sasa Jeshi la Polisi tumeshatangaza kuajiri askari wapya tutahakikisha kwamba kituo kile tutakifungua na tutapeleka askari ili wananchi waweze kupata huduma za ulinzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. FAKHARIA SHOMAR KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kwanza sina budi kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri na yanaleta faida kwa Watanzania. Hata hivyo nina maswali mawili madogo ya nyongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa uvamizi katika vituo vya Polisi siyo jambo jema, lakini nashukuru Jeshi la Polisi wameweza kudhibiti, lakini suala kama hilo huenda likajirudia. Swali langu linasema hivi: Je, ikitokea wamevamiwa katika vituo vyao na kwa bahati mbaya askari kajeruhiwa au askari kauliwa; familia ile inayomtegemea yule askari ambapo ndio tegemeo lao kimaisha, Serikali inawaambia nini au itawasaidia nini ili waweze kuishi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; kwa kuwa wanapovamia vituo, lengo kuu ni kupata zile silaha na kuwaathiri Polisi wenyewe walioko kituoni. Je, wakati wanapozungumza au wakati taarifa tunapozipata, baadhi yao wanazipata silaha; wanapokuwa wamezipata zinakuwa katika hali gani? Katika hali ya ubora ule ule wa awali au tayari zimebadilishwa ili wasiweze kuzitambua? Ni hayo tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Bi. Fakharia, Mbunge wa Viti Maalum, kutoka Mkoa Mjini Zanzibar, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Jeshi la Polisi kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi imeweka utaratibu maalumu wa askari wake watakapopata mitihani katika harakati za kulinda amani na utulivu wa nchi hii, lakini ni ikiwa imethibitika kwamba mtihani huo umemkuta ama ameupata akiwa katika harakati za kazi zake za kawaida za kiaskari. Kwa hiyo, kuna kanuni ya fidia ya pamoja ya Jeshi la Polisi na Magereza, hiyo hutumika. Katika kanuni hiyo imeelezwa viwango ambavyo huwa mtu anafidiwa kutokana na tatizo lililomkuta; kuna viwango akipata ulemavu, kuna viwango akikatika, na kuna viwango akifa. Kwa hiyo, Serikali kupitia Jeshi, imeweka utaratibu maalumu kupitia hii kanuni ambayo inawapa watu nafasi ya kuweza kupata fidia zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali lingine kwamba je, Silaha hizi tunakuwa tumezipata zikiwa zimeharibika au vipi? Silaha hizi zitakavyokuwa, zikiwa zimeharibika, zikiwa nzima, wajibu wetu tukizipata katika matukio ya kihalifu, maana yake ni kuzichukua. Kama itakuwa zimeharibika, maana yake tuna utaratibu wa kuzitengeneza. Ikiwa hazijaharibika, tunaiangalia; kama silaha ile ina kesi, tunaiacha kesi ile iendelee, ikimalizika, silaha ile inarudi Serikalini, inarudi jeshini, tunaendelea kuitumia kwa ajili ya Ulinzi na Usalama wa Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. ISSA A. MCHUNGAHELA: Mheshimiwa Spika, hali ya kufunga mpaka huu kwa muda mrefu imesababisha mkwamo mkubwa wa kiuchumi kwa wananchi katika eneo hili.

Je, hivi Serikali haioni sababu ya kufungua mpaka huu kusudi wananchi wanufaike na zile fursa zilizoko katika eneo lile? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Issa Ally Mchungahela, Mbunge wa Lulindi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge kama ataangalia zaidi katika jibu langu la msingi nimesema kwamba, ufunguaji wa kituo hiki unategemea zaidi makubaliano ya nchi mbili baada ya kukaa na kuangalia namna ya kuweza kufungua kituo hiki kwa ajili ya kuwapatia huduma wananchi. Nimesema Serikali inaendelea kufuatilia hali hii ili kuona namna bora ya kuweza kukaa na jirani zetu, ili kuweza kuwafungulia.

Mheshimiwa Spika, kikubwa afahamu tu kwamba, lengo letu kubwa ni kuhakikisha kwamba wananchi wanapata huduma katika mpaka huu katika hatua za uingiaji na utokaji na hali ya ulinzi na usalama inaendelea. Hivi tunavyozungumza vipo vikosi vyetu ambavyo vinaweka amani na utulivu katika eneo hilo na huduma nyingine zinapatikana. Ninakushukuru.
MHE. RAVIA IDARUS FAINA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Naibu Waziri.

Mheshimiwa Spika, NIDA walikuwa na mashine mbili za kuzalishia vitambulisho. Wakaomba kuongeza tena na mashine mbili kwa ajili ya kuzalisha vitambulisho vya Taifa. Sasa je, ni kwa nini uzalishaji na usambazaji wa vitambulisho hivyo umepungua kwa kiasi kikubwa sana na je, hawaoni wametumia fedha za wananchi vibaya sana?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Radhia Idarus Faina, Mbunge wa Jimbo la Makunduchi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulikuwa na mashine mbili ambazo zilikuwa zinazalisha vitambulisho vichache kwa muda mrefu, lakini tukaomba fedha kupitia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tukanunua mashine nyingine mbili na mashine hizi zikawa zinazalisha vitambulisho hivi kwa haraka kama ambavyo tofauti na mara ya mwanzo.

Mheshimiwa Spika, hivi ninavyokwambia shughuli za usajili, utambuzi na utoaji wa vitambulisho hivi unaendelea mpaka ilipofika tarehe 12 Oktoba, tulishakuwa na vitambulisho karibu 10,000,000 ambavyo viko tayari na muda wowote vinategemewa kwenda kusambazwa kwa wananchi. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba mashine hizi zinafanya kazi na vitambulisho vitapelekwa kwa wananchi hivi karibuni.

Mheshimiwa Spika, kuhusu kutumia fedha vibaya, hakuna fedha iliyoingia katika akaunti ya NIDA, aidha kwa Serikali au kutoka kwa wafadhili ikatumiwa vibaya. Hivyo nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, fedha zote zilizoingia kwenye akaunti ya NIDA zimetumika accordingly. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. MWANTUMU DAU HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, naomba kuuliza maswali yangu mawili ya nyongeza. Kwanza, nishukuru Serikali yangu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na mama Samia Suluhu Hassan jinsi anavyo chapa kazi mwanamama, kweli kinamama tunaweza. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Naibu Waziri na Serikali yake inatambua uchakavu huu wa majengo ya polisi ya Makunduchi pamoja na makazi na wametenga jumla ya shilingi milioni kumi na moja na tisini na tatu mia nne, ambazo fedha hizi zinatakiwa ziende zikafanye ukarabati katika majengo haya na vituo vya polisi.

Mheshimiwa Naibu Spika, vituo hivi vimechakaa sana, binafsi ukizingatia Makunduchi ni sehemu ya utalii hususan kila mwaka tunakwenda kule kukoga mwaka na viongozi wetu wakubwa wakubwa wanakwenda kule Makunduchi.

Kwa hiyo, je, Serikali lini itakwenda kuyatengeza majengo haya ili tuondoe kadhia hii ya majengo haya machakavu?

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala langu la pili, namuomba Mheshimiwa Naibu Waziri tena nasema tena, Mheshimiwa Naibu Waziri aende mwenye Makunduchi akayaone jinsi yale majengo pamoja na zile nyumba zilivyochakaa. Tuoneeni huruma jamani, tunaona vibaya? Ahsante sana naomba kuwasilisha. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NAMBO YA NDANIYA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba kujibu masuala mawili mazuri sana ya nyongeza yaliyoulizwa na Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kusini Unguja, Mwantumu Dau Haji nayajibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, moja miongoni mwa azma kubwa ya Serikali hasa kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kupitia Jeshi la Polisi ni kuhakikisha kwamba inaboresha na inatengeneza vituo vyote vya polisi vilivyopo nchini pamoja na nyumba za makaazi za maafisa hawa wa polisi na familia zao. Kwa hiyo, kubwa ni mwambie tu Kituo cha Makunduchi ni moja miongoni mwa kituo ambacho tumeshakipanga na tayari fedha hizi tumo mbioni kuzitafuta na kupitia mwaka wa fedha ujao tutahakikisha kwamba kituo hiki tunakipa kipaumbele ili kijengwe na shughuli za kitalii na mambo mengine yaweze kuendelea vizuri na shughuli za ulinzi na usalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo pia, nipo tayari kwenda Makunduchi kwenda kuona hilo eneo ili kuona namna ambavyo tunaweza tukashauri na tukaweza kupata fedha kwa ajili ya kukarabati hicho kituo. Nakushukuru.
MHE. DEODATUS P. MWANYIKA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Mkoa wa Njombe mpaka miaka michache iliyopita ulionekana kama ni mkoa mpya. Katika maeneo yaliyosahaulika kwa Mkoa wa Njombe ni Vituo vya Polisi. Je, Serikali ni lini sasa itaanza kukarabati Kituo cha Polisi cha Mkoa wa Njombe ili kiendane na hadhi ya Mkoa wa Njombe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda pia kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge kama ambavyo ameliuliza, linalozungumzia suala la ukarabati wa Kituo cha Polisi Njombe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba azma yetu ni kuhakikisha kwamba vituo vyote vinajengwa ipo pale pale. Lakini kikubwa nimwambie tu kwamba tutajitahidi pia katika mwaka wa fedha ujao tuhakikishe kwamba kituo hiki nacho tunakijenga kikawa katika hadhi ile ya kuhakikisha kwamba wananchi wanaweza kupata huduma hizi za ulinzi na usalama. Nakushukuru pia.
MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru, jengo la Kituo cha Polisi katika Mji Mdogo wa Mlowo ambapo mpaka sasa hivi tayari kimeishawekewa alama ya X kwa sababu kimejengwa kwenye hifadhi ya barabara.

Nilikuwa naomba kufahamu nini mkakati wa Serikali wa kutujengea Kituo kipya cha Polisi pale Mlowo na ikizingatiwa kwamba tayari tunalo eneo ambalo limetengwa pale Forest maalum kwa ajili ya ujenzi wa Kituo cha Polisi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shonza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli moja miongoni mwa changamoto ambazo tuko nazo ni kwamba vituo vingi vipo maeneo ya barabara na wakati Serikali inataka kutanua ama kupanua miundombinu ya barabara inabidi lazima kuna vituo vipitishwe doza kwa ajili ya kuvunjwa ili sasa barabara itengenezwe. Sasa nimwambie tu Mheshimiwa kwamba kwa kuwa eneo lipo, basi tutajitahidi tutenge fedha kwa ajili ya kujenga kituo hicho ili wananchi wa maeneo hayo waweze kupata huduma za ulinzi na usalama.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru pia.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushuku kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza. Ningependa kujua kituo cha polisi Mgeta ambacho niliahidiwa kujengwa na niliambiwa nilete tathmini ya ujenzi wa kituo hicho ambacho wananchi wamejenga, tumefikia kwenye boma. Waziri wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Naibu mwenye waliniahidi kwamba ikifika mwezi Agosti, 2021 kitakuwa kimeshamalizika kujengwa. Ni lini sasa watakwenda kumaliza hiyo ahadi yao?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mwita Getere nalo nalijibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba tulifika wakati tukaona kwamba tunaweza tukapata fedha haraka kwa ajili ya ujenzi wa kituo kile, lakini mambo yaliingiliana kwa sababu tuna nyumba za maaskari, tuna vituo vya polisi, tuna mambo mengi ambayo polisi tunahitaji tuimarishe ili wananchi waweze kupata huduma hizo. Kubwa nimwambie tu kwamba katika mwaka wa fedha ujao tutajitahidi kituo kile tukiangalie, tutakipa kipaumbele ili wananchi waweze kupata huduma za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. BONIPHACE N. BUTONDO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali la nyongeza. Wananchi wa Kishapu na wadau wa maendeleo katika Wilaya ya Kishapu wameanzisha jengo kwa maana ya Ofisi ya OCD ya Wilaya ya Kishapu na jumla ya shilingi milioni 60 zimetumika na jengo hilo lipo hatua ya renter. Sasa je, Seikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba ina-suport nguvu za wananchi na wadau ili mradi huduma za kipolisi ziweze kwenda sawasawa katika Wilaya ya Kishapu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba sasa nijibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Boniface nalo naomba nilijibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana kwa kuwa ni moja ya miongoni mwa watu ambao wanahamasisha sana wananchi ili kuweza kuanza ile miradi halafu Serikali kwa kupitia wafadhili tuje tuone namna ambavyo tunaweza tukamalizia. Kikubwa nimwambie kwanza, tutajitahidi baada ya Bunge hili tuje tuone hatua hiyo ambayo imefikia hicho kituo ili sasa tuone na sisi tathmini ya kuweza kujenga.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumwambie kwamba sasa tunakwenda kutafuta fedha, popote zilipo ili tuhakikishe kwamba kituo hiki tunakimaliza na wananchi waweze kupata hizo huduma katika maeneo hayo. Nakushukuru.
MHE. ALI HASSAN OMAR KING: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, hii habari ya vituo hayo yote tisa lakini kumi kuna Kituo Chukwani kimejengwa kwa nguvu za wananchi na kisha pauliwa tayari. Sasa ni ipi commitment ya Serikali ili kuja kumaliza kituo kile ambacho kinahitaji milioni 30 tu?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Ali Hassan King, Mbunge na Mtumishi wa wananchi wa Jimbo la Jang’ombe kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kiukweli ni kwamba kituo hiki tunakifahamu na binafsi nimeshakwenda kufanya ziara kwenye kituo hiki na hiyo amount ya fedha iliyotajwa tunaifahamu, kikubwa tulimwambia Mheshimiwa Mbunge ambaye alitupeleka katika eneo lile, ilikuwa ni Mheshimiwa Shaha. Mheshimiwa Ahmada Shaha tulikwenda kuona, kikubwa tulichomwambia kwamba sasa tunakwenda kutafuta fedha kwa sababu kama unavyojua siyo jambo la kusema kwamba tunachukua tu kesho tunakwenda kujenga. Ni jambo ambalo linahitaji taratibu za upatikanaji wa fedha kwa hiyo kikubwa nimwambie tu kwamba kituo hicho tunakifahamu na sasa tunakwenda kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniruhusu niulize maswali mawili madogo ya nyongeza, licha ya majibu mazuri yaliyotolewa na Wizara. Swali la kwanza; Jimbo la Vunjo ni jimbo lililo mpakani. Majimbo yaliyo mpakani yanakuwa na changamoto tofauti kidogo, kwa mfano, magendo na unajua Wachaga wanavyopenda magendo. Dawa za kulevya zinaingia halafu kunakuwa na uhamiaji haramu. Kwa hiyo, kuna umuhimu na tunaomba Serikali ituhakikishie kwamba, itachukua hatua gani ili kuimarisha ulinzi kwenye vituo vya polisi kwa kuongeza polisi pamoja na kuongeza bajeti kwa sababu, wanahitaji kuchukua za haraka wakati mambo kama yale yanapotokea?

Mheshimiwa Spika, swali la pili ni kwamba, kule Vunjo unywaji wa gongo, ulaji mirungi, bangi, dawa za kulevya umekithiri kwa sababu, of course watu hawana ajira wengi, lakini ukweli ni kwamba, imekithiri sana. Najua kwamba, Serikali za Mitaa zinafahamu jambo hili, lakini linahitaji national effort na tunataka tuombe Wizara iweze kutueleza inachukua mikakati gani ya kuweza kushughulikia tatizo hili la unywaji pombe kali, bangi na vitu vyote kama hivyo, otherwise tutapoteza kizazi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Vunjo, Dkt. Charles Stephen Kimei, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hatutasubiri mpaka tufike sasa watu waanze kuandamana. Serikali kupitia Jeshi la Polisi tuna mikakati madhubuti ambayo tumeifanya na tunaendelea kuifanya. Ya mwanzo, ni kuhakikisha kwamba, tunafanya doria za mara kwa mara ili lengo na madhumuni kuweza kukamata na kukomesha hizo tabia pamoja na kwamba, zinakuwa na changamoto kidogo, lakini tutajitahidi katika kuhakikisha kufanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, vilevile tunaendeleza sasa suala zima la ulinzi shirikishi; lengo na madhumuni sasa jamii iweze kutumia fursa ya kuchukua nafasi ya kuelimisha vijana wao ili sasa vijana waweze kupunguza hii, lakini kikubwa zaidi tunachukua hatua za kisheria. Kwa hiyo, wale vijana ambao wanafanya hili, basi tutawachukulia hatua za kinidhamu, hatua za kisheria, ili vijana waweze kuachana na tabia au vitendo vya utumiaji wa dawa za kulevya na utumiaji wa hiyo gongo kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Spika, nadhani maswali yalikuwa mawili, lakini yote yalikuwa yanaangalia kwenye gongo na bangi na masuala mengine. Nakushukuru sana.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Niseme nimepokea kwa furaha taarifa njema za magari 369 ya Polisi yatakayokuja. Swali langu. Je, katika magari hayo na ukizingatia kwamba, Kilimanjaro ina kata 169 na za mlimani ziko kama 110 zikiwemo kata za kule Siha, zikiwemo kata za Moshi Vijijini, Kata za Same, Kata za Mwanga na Kata za kule Rombo. Je, Serikali iko tayari sasa kupatia zile kata za mlimani ambazo haziko mjini magari hayo?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba, inasogezea wananchi huduma za ulinzi na usalama popote walipo. Moja miongoni mwa mambo ya msingi ambayo Serikali imeazimia kufanya kwanza ni kuhakikisha kwamba, tunatengeneza vituo vya polisi, lakini pili kuwatafutia magari ya polisi ambayo yatakwenda kufanya doria katika maeneo mengi. Nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, miongoni mwa maeneo ambayo yatafika haya magari tutajitahidi sana maeneo hayo ameyataja na huko kwenye mkoa wake magari haya yafike ili yaweze kutoa huduma. Nakushukuru.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, kwa kuwa, wananchi wengi wa maeneo ya pembezoni katika Jimbo la Kibamba, hasa maeneo ya Mpijimagohe kule Mbezi, Tegeta A kule Goba na maeneo ya Ukombozi kule Saranga, wameanza kujenga maboma ya vituo vya polisi kwa ajili ya usalama wa maeneo yao. Je, Serikali ni lini sasa itakuwa tayari kukamilisha maboma yale ili wananchi wale wapate usalama katika maeneo wanayoishi?
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu tena swali la Mheshimiwa Mtemvu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mambo yote ambayo yanaelezwa au vitu vyote ambavyo vinahitajika kwa ajili ya kufanyiwa wananchi kutoka katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, hasa kwenye Jeshi la Polisi, ni mambo ambayo yanahitaji fedha. Tukizungumza vituo vya polisi, fedha, tukizungumza magari, fedha, tukizungumza nyumba za askari, tunahitaji fedha. Nimwambie tu mheshimkiwa Mbunge kwamba, kwa sasa tunakwenda kutafuta fedha na tumeshaanza hiyo michakato ya utafutaji wa hizo pesa. Lengo na madhumuni ya kufanya hivyo ni ili tuweze kumaliza maboma yote nchini ambayo yanahitaji kumalizwa kuwawezesha wananchi kupata huduma za ulinzi na usalama. Nakushukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii kuuliza maswali ya nyongeza. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa wizi wa mazao ya kilimo na mifugo yamekuwa yakiongezeka pamoja na takwimu nzuri ambazo Mheshimiwa Naibu Waziri amezieleza hapa. Je, ningependa Mheshimiwa Naibu Waziri alieleze Bunge lako Tukufu tuna-fail wapi?

Swali Namba Mbili, ningeomba vilevile kuuliza kwa sababu kinga ni bora kuliko tiba. Je, hatuoni kwamba kuna haja ya kukinga haya matokeo ya wizi yasitokee ili kuwasaidia wananchi na wakulima wasiweze kupata hasara ya kuibiwa mazao yao. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mbunge wa wananchi wa Jimbo la Donge, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, Jeshi la Polisi wajibu wetu mkubwa ni kulinda raia na mali zao. Kwa hiyo katika hili tunajitahidi na tunafika hatua tunakuwa tunakutana na changamoto nyingi zikiwemo zile za wananchi wenyewe kwanza kushindwa kwenda kutoa ushahidi kwamba nani ameiba na nani amechukua mazao na nani amechukua mifugo. Lakini kikubwa ni kwamba tunaendeleza jitihada za kuhakikisha kwamba tunawakamata tunawafikisha kunako vyombo vya sheria hawa wanaohusika.

Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali katika kuzuia haya, tuna mikakati mingi ambayo kama atarejea kwenye jibu langu la msingi moja ni kuendeleza ule ushirikishwaji wa wananchi katika ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili ambalo pia tumelifanya kama ni sehemu ya mkakati ni kufanya doria za mara kwa mara katika maeneo haya hasa yale maeneo ya Zanzibar maeneo ya Donge, Muwanda na maeneo mengine ili lengo na madhumuni hivi vituko ama hivi vitendo vya uhalifu visiweze kutokea. Lakini kubwa nataka nitoe wito kwa wananchi wetu wasiendelee kuchukua hatua mikononi mwao, tumepata matukio mengi ya watu wanachinjwa, watu wanachomwa, watu wanachukuliwa hatua mikononi kitu ambacho ni kinyume na utaratibu wa sheria. Ninakushukuru. (Makofi)
MHE. NEEMA G. MWANDABILA: Mheshimiwa Spika, ahsate kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, Wilaya yetu ya Momba ina Halmashauri mbili. Halmashauri ya Mji wa Tunduma na Halmashauri ya Wilaya Momba. Makao Makuu yapo katika Halmashauri ya Wilaya ya Momba sehemu ambayo ni mbali kutoka Halmashauri ya Mji wa Tunduma, Katika hali ya usalama Tunduma ina hali hatarishi zaidi kuliko Wilaya ya Momba nilitamani kufahamu ni lini Serikali itaweka Wilaya mbili za kipolisi katika Wilaya ya Momba yaani Mji wa Tunduma pamoja na Halmashauri ya Momba. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu kwa kifupi sana swali la nyongeza la Mheshimiwa Neema Mwandabila kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, suala la uwekaji wa Vituo vya Polisi au uwekaji wa huduma hizi za ulinzi na usalama zinategemea mambo mengi sana, ukiwemo utaratibu wa kuangalia kwanza mahitaji ya eneo hilo, kwa sababu inawezekana kuna mahali vituo vipo karibu na huduma zipo karibu, lakini kikubwa ni kwamba nimwambie tutakwenda tukakague ili tuone kama tutaona kuna haja ya kufanya hivyo basi tutaweka. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nitauliza maswali pamoja na majibu hayo, nitauliza maswali mawili ya nyongeza kutokana na majibu ya Mheshimiwa Waziri, pamoja na kwamba amezungumiza suala la Kanuni za Magereza ambazo zinataka watoto watengwe tofauti na watu wazima wanapokuwepo Mahabusu. Mlundikano wa Mahabusu kwenye magereza zetu hauruhusu jambo hilo ni kwa nini sasa Serikali isiongeze au isipeleke Maafisa Ustawi wa Jamii ambao watakuwa wanashughulika na Watoto wanapokuwa kule kwa sababu ni vigumu sana ku-monitor. Kwa mfano, Gereza la Segerea kuna mahabusu si chini ya mia moja watoto na Maafisa wapo wawili tu ME na KE. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili; kwa nini sasa Serikali isipitie upya kujua idadi ya watoto ambao wana kesi kwenye Mahakama zetu na kwenye Mahabusu zetu yaani kwa maana ya Magereza ili sasa ile sheria kwa jinsi ilivyowekwa na ni nzuri, lakini utekelezaji wake ni mgumu ni kwa nini sasa wasipitie upya ili kuhakikisha kwamba watoto hawa wanasaidiwa kwa sababu hali za watoto wetu kwenye Magereza zetu ni mbaya mno. (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Nusrat Shaaban Hanje Mbunge wa Viti Maalum, nayo nayajibu kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Spika, kama Mheshimiwa atarejea kwenye jibu langu la msingi atagundua kwamba kuna sehemu nimesema kutakuwa kuna Maafisa wa Ustawi ambao watakuwepo maalum katika magereza kwa ajili ya kusimamia haki na maslahi na kuwalinda watoto hawa. Kwa hiyo, kama changamoto ni Maafisa hawa kuwa kidogo basi nimhakikishie tutajitahidi Serikali kupitia Jeshi la Magereza ili kuona kwamba tunaongeza Maafisa hawa ili watoto wetu waweze kupata huduma nzuri za kuweza kusaidiwa na Maafisa hawa pamoja na kwamba kuna nafasi nyingine ya kushughulikiwa na wazee wao na mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kingine Mheshimiwa amegusia suala la kwa nini isipitiwe upya sheria au tuone namna, nimwambie kwamba sheria hii kwamba ipo vizuri, lakini kwa kuwa na yeye ameshauri tuipitie upya basi tutakaa tutaipitia sheria hii ili kama kutakuwa kuna mapungufu basi tutajua namna ya kuifanyia marekebisho.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)

MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI: Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge pia aliuliza umuhimu wa kujua idadi ya kesi za watoto. Kesi zote zinazokwenda Mahakamani zinasajiliwa kwa namba, kwa hiyo kama atauliza swali mahsusi kwa Mahakama maalumu au kwa Gereza maalum idadi hiyo itapatikana kwa namba na kwa majina ya wahusika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili; Sheria ya Mtoto ya Mwaka 2009 inaweka misingi ya kulinda maslahi ya mtoto. Kwa hiyo, kwa mtu aliyechini ya kizuizi cha magereza anapopelekwa mahakamani kama hapati huduma inayostahili akiwa magereza anayohaki ya kutoa hiyo hoja kwa Hakimu ambapo shauri hilo lipo mbele yake na maelezo ya kisheria kwenda kwa wanaosimamia hizo selo yakatolewa. Nninakushukuru. (Makofi)
MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia fursa ya kuuliza swali. Katika kulinda haki za watoto ni lazima au ni sharti tuzingatie wale watoto ambao unakuta hawana kesi, bali mama zao aidha wameenda wakiwa wajawazito au wamekamatwa ni mahabusu au mfungwa akiwa na mtoto ambaye yuko chini ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Spika, katika Gereza la Segerea tumeshuhudia wamama wanakuja na watoto wao pale wa jinsia tofauti, lakini wanachangamana na watu wazima. Kwa hiyo, unakuta mtu mzima labda anataka kwenda kuoga anavua nguo, yuko hivi na mtoto yuko pale. Tunajua kwamba makuzi ya watoto ubongo wao ni kuanzia miezi sifuri mpaka miaka mitano. Kwa hiyo, unakuta unam-affect kisaikolojia.

Mheshimiwa Spika, nataka kujua sasa, ni hatua gani Serikali inachukua kuhakikisha kwamba wale mahabusu au wafungwa ambao wamekwenda wakiwa wajawazito, wamejifungua wakiwa Magereza au wameenda na watoto wachanga, waweze kutengwa kwenye cell special ya akina mama wenye watoto au wajawazito wasiweze kuchangamana na hawa watu wengine? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Esther Matiko kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kuna hatua nyingi ambazo huwa zinachukuliwa. Huo utaratibu upo na upo tangu zamani. Inawezekana tu labda kuna maeneo yeye ameyashuhudia, ameona kwamba watu wanachanganyika na wengine wanakuwa wanataka labda pengine… kama hivyo. Kikubwa nimwambie kwamba ziko hatua ambazo Serikali inazichukua ikiwemo ya kuwatenganisha ili sasa ikitokea hali kama hiyo, waweze kupatiwa msaada maalum. Ziko hatua nyingi tu ambazo tunazichukua kama Serikali na kama Jeshi la Magereza. (Makofi)
MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Spika, majibu haya yaliyoletwa haya reflect kabisa hali halisi iliyoko Jimboni Ndanda na Kwenye Kijiji cha Namajani hasa zaidi kwenye Vijiji wa Ngalole, Namajani, Kijiji cha Pangani na Matutwe pamoja na Mahinga.

Mheshimiwa Spika, utakumbuka swali hili nilileta kwa mara ya kwanza 2016 na majibu yaliyotolewa yanafanana na kesi hii wanakijiji hawa walishinda mahakamani mwaka 2012 na mara nyingi wizara wamekuwa wanajitetea kwa kusema kwamba wanafanya tathimini na wanatafuta pesa. Kwa mara ya mwisho wamefanya tathimini mwaka jana kabla hatujaingia kwenye bajeti kuu na hakuna pesa yoyote iliyotengwa na Serikali kwa nia ya kwenda kuwalipa kwa hiyo nina amini hawana nia njema sana ili kulimaliza jambo hili. Mgogoro uliopo sasa ni wa malipo.

Sasa swali langu kama Serikali au Magereza wameshindwa kulipa fedha hii hawaoni sasa kuna haja ya ku-vacate na kuondoka eneo hili wakawaachia wananchi wafanye shughuli zao?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwa sababu imekuwa ni muda mrefu sana endapo Mheshimiwa Waziri sasa atoe commitment kwamba kufikia lini jambo hili litakuwa limekwisha na wananchi wale watakwenda kupata stahiki zao. Ahsante.
NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Cecil David Mwambe Mbunge Ndanda kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka tu tuone namna ambavyo tunaweza tukaondoka hapa katika eneo hili, lakini nimwambie tu kwamba waliokuwepo hapa ni chombo cha Serikali ambacho kwa kusema tu tuondoke tu kirahisi rahisi nimwambie hili kwamba ni jema lakini inabidi sasa tukae tuone namna itakavyowezekana kwa sababu waliokuwepo hapa ni Jeshi na wanashughulikia wananchi na wanasaidia kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, lakini Je, lini hili jambo litakwisha akisoma katika jibu langu la msingi ni kwamba Tayari tumeshaanza hatua kwanza za uhakiki kujua nani anastahili kulipwa na nani hastahili kulipwa zaidi ukizingatia kwamba mahakama amri hapa mahali sisi tuondoke. Kikubwa ni kwamba tunaenda kutafuta fedha kwa sababu hizi fedha siyo kidogo ili tuweze kuwa compensate hawa waliokuwepo basi tuone namna itakavyowezekana, nakushukuru.
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwanza tunaunga mkono jitihada za Serikali. Hata hivyo, kuna wananchi ambao wanafanya shughuli zao za kilimo cha mbogamboga ambazo zinawaingizia kipato, wako ndani ya mita 60; na shughuli zao hizo haziathiri mazingira.

Je, Serikali iko tayari kuwasaidia wananchi hao au kuwalinda ili wazidi kujiongezea kipato?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa eneo hili linaweza likageuzwa kuwa vivutio au sehemu ambazo ni center ambazo wananchi wanaweza wakatengeneza, kama vile Coco Beach au sehemu nyingine, wakaweza kupata shughuli za kujiendeshea maisha yao.

Je, Serikali iko tayari kuwasiliana na Halmashauri zetu ili wananchi wetu ambao wanaweza kufanya shughuli hizi waweze kupewa maeneo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge wa Jimbo la Segerea kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili jambo la mita 60 ni jambo la kikanuni kabisa. Lakini kingine tunaweza tukawaruhusu wakaendelea ndani ya mita 60; lakini changamoto iliyopo, athari za kimazingira si athari za kuonekana leo na kesho. Huwezi ukachimba mgodi leo, ukawa unachimba dhahabu au chochote ukaziona athari leo. Huwezi kukata miti ukaona athari leo, huwezi ukaendesha viwanda ukaona athari leo. Kwa hiyo ni jambo ambalo ni la muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa leo na kesho inawezekana wananchi wa Segerea wanaweza wasione athari za kimazingira, lakini baada ya muda watakuja kuona athari za kimazingira. Hicho ndicho kitu ambacho sisi Serikali tunakihofia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ni vipi tutawasaidia, tuko tayari kuwasaidia kwa kuendelea kuwapa taaluma ili sasa waweze kufahamu mambo haya ili wajue athari za kimazingira. Kwa sababu tusipoyalinda mazingira hayataweza kutulinda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali lingine kwamba je, Serikali iko tayari kuwatengenezea creation centers kwa ajli ya angala ya kuweza kujiendesha. Hilo jambo wala hatuna tatizo nalo kwa sababu lengo letu ni kwasaidia wananchi; lakini nadhani watupe muda kwanza ili tutafute fedha kwa sababu hili jambo linahitaji fedha. Kupageuza pale ili tutengeneze sehemu ya kivutio yenye garden nzuri tunahitaji tupate fedha za kutosha. Lakini pia watupe muda ili tuweze kufanya ushauriano na baadhi ya wadau wengine maana pale Wizara za Maji, Maliasili na Ardhi, pamoja na sisi na Halmashauri zinahusika. Kwa hiyo jambo hilo linawezekana, lakini watupe muda kidogo ili tujue namna ambavyo tunafanya. Nakushukuru.
MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru; kwa kuwa leo ni Siku ya Saratani Duniani, ningependa kuiuliza Serikali, ina mkakati gani wa kuzuia wenye viwanda ambao wanachepusha machi yenye kemikali ambazo si salama? Maji haya yanakwenda kwenye Mto Msimbazi na ndiyo maji hayo hayo ambayo hawa wakulima wa mbogamboga wanatumia katika kuzalisha na kumwagilia mbogamboga hizi, hivyo kuhatarisha usalama wa chakula (food safety) na hatimaye usalama wa hali ya afya ya wananchi na hivyo uwezekano wa kuchangia katika saratani ni mkubwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba majibu.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tena kujibu swali la Mheshimiwa Neema kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumebaini kuwa kuna baadhi ya shughuli nyingine za kibinadamu zinasababisha uchafuzi wa mazingira, zikiwemo hizo ambazo amezitaja, za viwanda na nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi kama Serikali kupitia Ofisi ya Makamu Rais, Muungano na Mazingira tunazo jitihada Madhubuti ambazo huwa tunazichukua katika kuhakikisha kwamba tunazuia mambo haya ili kuweza kuzuia athari kwa wananchi, ikiwemo hiyo milipuko ya maradhi, yakiwemo ya kansa na mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, tunaendelea kutoa taaluma kwa hawa wanaofanya shughuli hizi za kibinadamu, lakini la pili kuna wakati tunatoa hata faini ili waweze kuacha na iwe funzo kwa wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile huwa tunafanya operations za mara kwa mara kwenye haya maeneo ya uzalishaji, lengo na madhumuni ni kwamba wanaozalisha wajue kwamba wanazalisha lakini wananchi nao wanaathirika. Lakini zaidi tunafika hatua mpaka tunazuia. Inafika wakati kuna kiwanda kinafanya visivyo, kuna shell inafanya isivyo, kuna migodi inafanya visivyo. Kisheria, kwa mujibu wa utaratibu tunazuia uzalishaji ili sasa shughuli nyingine au taratibu nyingine za uhifadhi wa mazingira ziweze kuendelea. Nakushukuru.
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na ukosefu wa taaluma za kimazingira katika Bonde la Mto Msimbazi ambayo husababisha uchafuzi wa kimazingira kutokea, hali kadhalika ukosefu huu wa elimu unawahusu hasa wavuvi ambapo bahari yetu imechafuka sana na tunakosa samaki wenye afya kutokana na wavuvi kwenda na plastics na vitu vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusikia Serikali ina mkakati gani, kwanza kuisimamia rasilimali hii muhimu ya bahari, lakini la pili, kutoa taaluma kwa wavuvi wetu ili rasilimali yetu iwe salama?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sasa kujibu swali lingine la Mheshimiwa Asya, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kazi kubwa tunayofanya kama Serikali na kama Wizara hii ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira ni kuwapa wananchi elimu; na ni kwa sababu tumefika wakati tumegundua kwamba elimu pekee ndiyo itakayotuokoa sisi kutokana na mazingira machafu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa wavuvi tumefanya jitihada kubwa. Kaskazini Unguja, kwa sababu kuna bahari tumewapa elimu, Kaskazini Pemba, Kusini Pemba na maeneo yote ya Tanzania yenye visiwa, mito, maziwa pamoja na bahari ambamo shughuli za uvuvi zinafanyika tumejitahidi sana tumewapa taaluma na taaluma inafanya kazi, na tutandelea kufanya hivyo. Nakushukuru.
MHE. VITA R. KAWAWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana; kwa kuwa kulikuwa na wananchi ambao walipata silaha hizo kihalali na kwa kufuata taratibu zote na walikuwa wanazilipia kila mwaka na wenyewe walitii amri kwa kuzipeleka katika vituo vya polisi na sasa Serikali imeamua hivyo isiwarudishie. (Makofi)

Je, Serikali inaweza sasa kuwarudishia thamani ya gharama ya silaha zao? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa Jimbo la Namtumbo ni la wakulima na mashamba yao yamezungukwa na mapori yenye wanyama wakali na waharibifu na kwa kuwa Serikali awali dhamira yake iliwaruhusu kuwa na silaha hizo ili waweze kujilinda wao wenyewe na mali zao ambayo ni mashamba yao.

Je, Serikali sasa ina mpango gani mbadala wa kuweza kuwasaidia wakulima na wananchi hawa, kuepukana na adha wanayoipata ya kuharibiwa mazao yao na kuuawa na wanyama waharibifu na wakali? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Kawawa, Mbunge wa Namtumbo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Kawawa, lakini pia niwapongeze sana wananchi wa Jimbo la Namtumbo kwa kuendelea kuwa na subira kwa jambo hili. Wamesubiri kwa muda mrefu lakini nataka niwaambie wananchi na Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali na lengo lake ni kulinda raia na mali zao. Tunaposikia mahali kuna majangili, kuna majambazi, kuna magaidi, kuna watu ambao aidha wanataka ama wanafanya shughuli ama mambo ya uvunjifu wa amani, sisi kama vyombo vya ulinzi na usalama wajibu wetu ni kuhakikisha kwamba tunakwenda kutuliza na ikiwezekana kukamata kila kinachohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukitazama hili jambo suala la uchunguzi sio jambo la kusema kwamba tunafanya leo na kesho na silaha zimetajwa hapa katika jibu la msingi ni karibu 1,579. Lakini hazikukamatwa silaha tu kuna wahalifu waliokamatwa na silaha hizi sio hizi silaha hizi tu kuna visu, kuna mapanga na nyinginezo. Nadhani wengi wenu mnakumbuka zile operesheni za Kibiti na nyingine.

Kwa hiyo, nimuombe Mheshimiwa Mbunge pamoja na wananchi wake waendelee kuwa na subira. Serikali kupitia vyombo tunafanya uchunguzi kuhakikisha kwamba nani anayehusika na silaha ipi inahusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu ukiangalia katika masuala ya investigation sio jambo la kusema tunafanya leo, kesho tunapata majibu na ndio maana watu wengi walilalamika jambo linachukua muda mrefu kuchunguzwa kwa sababu tunataka tutende haki.

Lakini swali la pili je, sasa Serikali ina mpango gani mbadala kusaidia kupunguza sasa hizi adha za wanyama pori. Nataka niendelee tena kumuambia Mheshimiwa Kawawa pamoja na wananchi wa Jimbo hili kwamba Serikali imekuwa ikifanya operesheni na misako mbalimbali ya kusaka hawa watu wahalifu. Lakini pia kuwasaidia kuepukana na madhara ya hawa wanyama pori.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vilevile kumekuwa kuna Jeshi letu hili linaloshughulika na masuala ya wanyama pori wanaweza pia tukawasaidia kupitia hili. Vilevile Serikali tumetoa namba maalum hasa kwa wale watu ambao wanafanya kazi za kilimo na shughuli nyingine katika misitu, lengo na madhumuni ikitokea mtihani wowote waweze kutuambia. Tuendelee kuwaomba radhi na kuwaambia wananchi wasubiri jambo linafanyiwa ufuatiliaji. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. OMAR ALI OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri nina maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza ni kwamba kutokana na gharama ya fedha ambazo zimetengwa kwa ajili ya ukarabati wa jengo hilo ambalo alisema kwamba ni chakavu lakini jengo hilo ni bovu kabisa.

Je, haoni Mheshimiwa Waziri kwamba kuna haja sasa ya kuambatana na mimi kwenda katika jengo hilo kwenda kujionea na kuona uhalisia wa gharama zinazohitajika katika kutengeneza jengo hilo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti swali langu la (b) ni kwamba kutokana na ongezeko la vitendo vya udhalilishaji na vitendo mbalimbali vya unyanyasaji wa wanawake na watoto katika eneo la Mkoa wa Kaskazini Pemba na magari ambayo yanatumika ni magari matano tu. Haoni kwamba kuna haja sasa ya kuweza kuongeza magari ya dharura kwa ajili ya kuhakikisha kwamba vitendo hivi vinakomeshwa muda mfupi ujao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Omar, Mbunge wa Jimbo la Wete kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya miongoni mwa wajibu wetu mkubwa ni kuhakikisha kwamba tunakwenda kuona kila jengo ikiwa nyumba za makazi, Kituo cha Polisi, mradi wowote ambao unashughulika na masuala ya Jeshi la Polisi ni wajibu wetu kwenda kuukagua. Nimwambie tu Mheshimiwa Omar kwa kushirikiana na wananchi wa Jimbo la Wete tupo tayari kama Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwenda kukagua na kuona na sio Wete tu, lakini maeneo yote ya Unguja na Pemba na Tanzania kwa ujumla. Ni sehemu ya wajibu wetu na tuko tayari kufanya hivyo na mimi niko tayari kuambatana na yeye.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine je, sasa si tupate hata gari kwa ajili ya doria na vitendo vya uhalifu? Nimuambie tu Mheshimiwa katika bajeti ambayo tumeisoma ya mwaka 2021/2022 tulisema kwamba tuna jumla ya magari zaidi ya 300 ambayo yatakuja kwa ajili ya Jeshi la Polisi. Nimuambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Jimbo la Wete tutaliangalia kwa jicho la huruma sana kuhakikisha kwamba gari hizo zinakwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri na yenye matumaini mazuri, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa vile mchakato wa wenzetu hawa NEMC kujiunga na Mfuko wa Fedha wa Green Climate Fund umechukua muda mrefu kuliko ilivyotaratijiwa; na kwa kuwa sehemu ya mchakato huo ilishafanyika wakati NEMC wanajisajili katika Mfuko wa Adaptation Fund.

Je, NEMC wamejipanga vipi kuweza kuainisha vipaumbele vya miradi kwa kuzingatia maeneo ya kijiografia, Zanzibar na Tanzania Bara ili wakishapata usajili wasije tena kuchelewa kuwasilisha andiko la mradi kwenye sera hizi ambazo nchi mbalimbali zinaomba na hazijatengwa kwa ajili ya Tanzania peke yake?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kwa kuwa tunaenda kupata taasisi ya pili sasa kwa upande wa Tanzania Bara ambayo imepata accreditation kwa upande wa Mfuko wa Fedha wa Green Climate Fund: Je, Ofisi ya Makamu wa Rais imejipanga vipi kuisaidia Zanzibar angalau kuweza kupata taasisi moja ambayo itapata usajili kwa ajili ya Mfuko huu wa Mabadiliko ya Tabianchi ili Wazanzibar nao wawe na direct access ya kuomba hizi fedha za mabadiliko ya tabianchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumjibu Mheshimiwa Soud maswali yake ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Soud kwa kazi nzuri anayoifanya hasa ya kutoa elimu kwa wananchi katika masuala mazima ya uhifadhi wa mazingira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo maeneo ambayo tumeshayaainisha au tunayafanya kabla hatujaanza kufanya uteuzi wa hiyo miradi. Kwanza huwa tunatembelea maeneo ambayo tunaweza tukaiibua hiyo miradi ambayo tunaweza kuiingiza huko. Kingine tunachokifanya ni kukusanya taarifa ambazo zinaweza kusaidia na baadaye tunaenda kuziandikia project proposal.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto iliyokuwepo hapo ni kwamba mara nyingi miradi hii inakuwa inasuasua. Kwa hiyo, nataka nichukue fursa hii nitoe wito kwa Wakurugenzi wote wa Halmashauri nchini, wajitahidi wasimamie vizuri miradi hii, kwa sababu kuna baadhi ya maeneo fedha zimepelekwa, lakini bado miradi hii inasuasua haijamalizika utekelezaji wake wakati bado kuna baadhi ya maeneo miradi hii imeshakamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu kuisaidia Zanzibar kupata angalau taasisi; Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira ipo wazi, kikubwa ni kwamba tunawaomba waje, tutawaelekeza, tutawafahamisha, tutawaambia namna ambavyo tunaweza tukawasaidia wakaingiza hizo taasisi. Kikubwa ni kwamba wanaweza wakaandaa pia miradi ili wakija kwetu inakuwa rahisi kuifanyia utekelezaji. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri ambaye anahusika na Mazingira katika Kikao cha Bunge kilichopita alitoa ahadi ya kuja kutembelea Kisiwa cha Pemba ili kuona athari ya mabadiliko ya tabianchi hasa katika Kisiwa cha Mtambwe Mkuu, Kojani na Kisiwa Panza.

Je, ni lini hasa atakuja kuona athari hiyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshiwa Naibu Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Khalifa kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba baada ya Bunge hili tukijaaliwa tutajitahidi tupange ziara kwa ajili ya kwenda Kojani na maeneo mengine ya Mtambwe Mkuu kwenda kukagua maeneo hayo. (Makofi)
MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, mabadiliko ya tabianchi yamesababishwa sana na uharibifu wa mazingira; na mara nyingi ukipita katika milima hii ya Kitonga, Nyang’oro pamoja na kule Makombe unakuta kwamba watu wamekuwa wakichoma mkaa ovyo: -

Je, Serikali ina mpango gani wa kuweka ulinzi sasa kwenye misitu hii ili uharibifu wa mazingira usiendelee. Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo mikakati mingi tunayoipanga katika kuhakikisha kwamba tunalinda mazingira, hasa katika maeneo hayo. Moja ni kwamba tunaendelea kutoa taaluma kwa wananchi kama sehemu ya wajibu wetu kuhakikisha kwamba wananchi hawaendelei na uharibifu wa mazingira.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine kikubwa tunachokifanya, tunayo majeshi yetu kule au walinzi wetu ambao tunashirikiana nao na vikosi vingine vya ulinzi pamoja na Jeshi la Maliasili ambao mara nyingi huwa tunajitahidi kushirikiana nao kulinda mazingira katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Napenda kumpongeza Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa mashirikiano haya hayapo kisheria: Je, Serikali haioni haja ya kuwa na utaratibu wa kisheria ili kuwezesha ushiriki wa Zanzibar kuwa bora zaidi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali la pili: Je, mpaka kufikia Julai, 2022, Zanzibar imenufaika na miradi gani ya kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kusini Pemba, Mheshimiwa Maryam Azan Mwinyi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ushirikiano na majadiliano ambayo huwa tunafanya yanayohusiana na mikataba ya Kimataifa, ya mazingira na kukabiliana na mazingira ya tabia ya nchi, ni ya kisheria. Maana yake, yako kisheria. Hata ukienda ukisoma Katiba ya Jamhuri kwenye fungu lile la Foreign Affairs utakuta kumeelezwa namna ambavyo inatakiwa tushirikiane kwenye mahusiano yanayohusu masuala ya mikataba ya Kimataifa.

Mheshimiwa Spika, hata ukienda kwenye sheria yetu ya mazingira, imeeleza, Waziri anayehusika na mazingira kwa upande wa Jamhuri ya Muungano, basi anatakiwa akae na ashirikiane na Waziri anayehusika na mazingira kwa upande wa Zanzibar. Kwa hiyo, majadiliano haya hasa mikataba ya Kimataifa yanakuwa yapo kisheria zaidi.

Mheshimiwa Spika, ipo miradi ambayo imetekelezwa na inaonekana. Kwa mfano, kuna ujenzi wa kuta ama kingo za kuzuia maji Wete kule Sepwese, hiyo ipo; pia kuna miradi ya kurejesha ardhi iliyoathirika na mabadiliko ya tabia ya nchi, hii iko maeneo ya Kiuyu, Shumba Viamboni, Shumba Mjini, Maziwa Ng’ombe maeneo mingine miradi hii ipo na imepita.

Mheshimiwa Spika, pia upo mradi wa kukabiliana na mabadiliko ya tabia ya nchi maeneo ya Kaskazini A, Unguja katika Mkoa wa Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, nashukuru.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; je, katika kuandaa mwongozo huo TFS ambao wamekuwa na migogoro na wananchi wanaozunguka hifadhi hizo za misitu wameshirikije?

Swali la pili; je, Serikali haioni haja ya kushuka kwa wananchi na kutoa elimu ya biashara ya hewa ya ukaa ili kujenga ufahamu zaidi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA
MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felix, Mbunge wa Buhigwe, najibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba moja miongoni mwa wadau ambao watakuwa ni sehemu kubwa ya mwongozo huo ni TFS na nimwambie kwamba tumewashirikisha vya kutosha katika mwongozo huu na siyo wao tu; tumeshirikisha taasisi nyingi za kibinafsi na za Serikali, lakini zaidi tumewashirikisha sana Tawala za Mikoa wakiwemo Halmashauri, Majiji, Wilaya, Mikoa na Vijiji ili lengo na madhumuni na wao wawemo katika sehemu ya mradi huo ili watusaidie katika kuwaeleza wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa kuwafikishia taaluma wananchi, hili jambo ni la mwanzo tumelipa kipaumbele na tayari timu ipo imeelezwa katika mpango huo, kutakuwa na timu maalum ambayo itapita nchi nzima kuzunguka kwa ajili ya kutoa kwanza elimu kwa wananchi wafahamu mradi huo na faida zake, lakini wafahamu fursa zinazopatikana katika mradi huo, lakini wafahamu faida za kimazingira ambazo zitapatikana katika mradi huu. Nakushukuru.
MHE. LATIFA KHAMIS JUWAKALI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, nikushukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu mazuri ambayo yanakwenda kuwatia moyo wananchi.

Kwa kuwa suala hili Wizara mmesema kwamba lipo katika mchakato na wananchi hawa bado sasa hivi wanaendelea kuwa na matumaini makubwa, lakini bado wanakosa kushiriki shughuli zao za kiuchumi ikiwa suala la kilimo, suala la ufugaji kwa sababu tayari walishafanyiwa tathmini.

Je, Serikali mnatoa kauli gani kwa wananchi hawa ili waendelee kuwa na matumaini?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili, Mheshimiwa Waziri wananchi hawa itakapokuwa imetoka hiyo fidia; je, muda huo ambao mtakuwa tayari mmeitoa hiyo fidia inakwenda kuendana na thamani ya fedha katika kipindi hicho yaani value for money? Nakushukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kusini Unguja, Mheshimiwa Latifa Khamisi Juakali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia katika jibu la msingi tayari kuna majibu yanayowapa wananchi matumaini, niwaambie tu Mheshimiwa Mbunge wananchi waendelee kuwa na matumaini kwa sababu azma ya Serikali hii ni kuhakikisha kwamba tunaondosha migogoro yote ambayo inakabili baina ya vyombo vyetu vya ulinzi na wananchi; na ndiyo maana katika jibu la msingi tukasema kuna majadiliano yanaendelea baina ya SMZ na Jeshi la Wizara ya Ulinzi. Lakini pia tukasema kwamba tayari tumeshaomba fedha kwa ajili ya kuwalipa fidia. Kwa hiyo, Mheshimiwa ahakikishe watu wake wanaendelea kuwa na matumaini.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine kikubwa ni kwamba tutahakikisha kwamba thamani zitakwenda kwa mujibu wa mali zao, ikiwa vipando, ikiwa nyumba, lakini Serikali haitawadhulumu, itahakikisha kwamba wanapata kile ambacho wanastahiki. Nakushukuru.
MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi, mwaka 2020 Mheshimiwa Waziri wa Mazingira alifanya ziara kule Ziwa Bassuto na aliahidi kwamba atatuma timu ya wataalam ili waje kufanya tathmini kuona namna gani wanaweza kudhibiti madhara yanayoendelea kuwapata wananchi wa eneo hilo. Lakini kwa majibu haya ya Serikali sasa wananchi wategemee nini?

Mheshimiwa Spika, kipengele cha pili, ni lini Serikali sasa itatafuta fedha kwa ajili ya kuboresha mazingira ya Ziwa Bassuto kwa sababu wananchi wale wanaendelea kupata madhara makubwa ili kuepuka yale madhara yasiendelee kuwapata wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza Mheshimiwa Mbunge Regina Qwaray, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali haina kauli mbili, kauli ya Serikali ni kauli moja, sasa katika hili namuomba Mheshimiwa Mbunge, twende na hii kauli ya kwamba kwa sasa hivi Serikali hatujawa na mpango wa kufanya kama vile Mheshimiwa anavyosema kwa sababu kama ambavyo tumeeleza katika jibu la msingi.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa upande wa fedha nadhani hili sasa atupe muda tuona namna ya kukaa na kushirikiana na baadhi ya Wizara zingine za kisekta, ikiwemo Wizara ya Kilimo, Wizara ya Maji na Wizara yetu ya Mazingira ili kuona namna ambavyo tunaweza kujadili kwa pamoja na baadaye tukatafuta fedha kwa ajili ya ziwa hili.
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini sasa taarifa hiyo ya tume itawekwa wazi kwa wadau na wananchi wote kuifahamu na kuijua?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, migongano na migogoro hii imesababisha wananchi kujichukulia sheria mkononi, na je, Serikali haioni haja ya kuja na mkakati wa pamoja kama Serikali mkakati wa haraka kuhakikisha namna gani tunakabiliana na hii changamoto ya watu kujichukulia sheria mkononi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Cecilia Daniel Paresso, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kama ambavyo tumesema katika jibu letu la msingi kwamba kufuatia kuongezeka kwa matukio haya tayari Serikali imeunda tume ama timu maalum kwa ajili ya kuchunguza na kuweza kuleta majibu.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba kweli timu iliundwa na taarifa zimekuja, majibu yamekuja lakini bado Serikali tunaangalia kama kutakuwa kuna haja ya namna ya kuweza kutoa hizi taarifa kwa jamii basi zitatolewa. Kama hatuna namna basi tutaona namna nyingine ya busara zaidi ya kuwafikishia majibu wananchi ya tume hii iliyoundwa kwa ajili ya kuchunguza hayo matukio.

Mheshimiwa Spika, lingine ni kuhusiana na mkakati, ama bila ya shaka kuna haja ya kuwa na mkakati na mkakati upo, na mkakati wa kwanza katika hili ni kuendelea kuwaelimisha watu. Moja kuhusiana na masuala haya ya kishirikiana, kwamba si kila ambaye anakuwa na sababu hizo maana yake auliwe. Lakini kingine ni kushurutisha sheria kwamba watu lazima wafuate sheria na wasijichukulie sheria ama hatua mikononi mwao. Nashukuru.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kuniruhusu kuuliza swali la nyongeza.

Kwanza nikiri kwamba Serikali imefanya kazi kubwa sana Wilayani Kilosa na nimpongeze DC wa Wilaya Kilosa Alhaji Majid Ahmed Mwanga kwa kazi kubwa ya kupunguza na kuondoa kabisa katika baadhi ya maeneo migogoro kati ya wakulima na wafugaji.

Mheshimiwa Spika, lakini pamoja na hayo kwa namba hizi ambazo naziona na ripoti nyingi za matatizo ya wakulima kulishiwa mazao yao katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu. Je, nini mkakati wa Serikali wa kumaliza matatizo haya?

Pili, Serikali haioni wakati umefika sasa wa kulichukulia jambo hili kama janga la kitaifa Wizara ya Mambo ya Ndani ikae na Ofisi ya Waziri Mkuu kuona namna bora ya kulichukulia suala hili kama janga? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dennis Lazaro Londo, Mbunge wa Mikumi maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Jeshi la Polisi na vyombo vingine vikiwemo vya Mahakama kwa kweli tumechukua hatua nyingi na tofauti, moja tumegundua kwamba bado kuna watu uelewa wao ni mdogo katika hili. Kwa hiyo cha kwanza ni kuendelea kuwapa taaluma wananchi juu ya suala hili, lakini kingine tunaendelea kutoa maelekezo kwa baadhi ama kwenye vyombo mbalimbali ikiwemo watu wa halmashauri, watu wa miji na majiji ili kuendelea kutusaidia kulilea suala hili ili kuhakikisha kwamba mambo haya yanaondoka kabisa katika jamii.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa upande mwingine nikiri kwamba kweli hili suala ni janga na kwa sababu linarudisha nyuma hali za wananchi zikiwemo hali za kiuchumi na mambo mengine kwa hiyo kutokana na hali hii ndiyo maana sasa tukaona pia bado kuna haja ya kuchukua baadhi ya mikakati na hatua hizi. Kwa hiyo nikiri kwamba hili ni janga na kwa sababu linawaathiri sana wananchi.
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwakuwa eneo hili kuna baadhi ya maeneo tayari yana miundombinu ya umwagijiaji na miundombinu hii ipo ardhini na ikikaa kwa muda mrefu inaweza kuharibika nataka kujua: -

Je, ni lini hasa Serikali itatenga kiasi hichi cha Shilingi bilioni 11.5 ili kunusuru miundombinu hii?

Mheshimiwa Spika, swali la pili kwakuwa maeneo mengi nchini katika mikoa yetu yana madhari yanayofanana na Mngeta na maeneo ya Chita.

Je, Serikali haioni kuwa ni wakati sasa wa kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji kwa pamoja ili kupambana na uhaba wa chakula pamoja na kuendeleza usalama wa chakula nchini? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Felista Deogratius Njau, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Dar es Salaam. Kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana kwa kazi nzuri anayoifanya katika mkoa wake, lakini pia kwa hamu aliyonayo ya kuona kwamba siku moja jeshi hili linazidi kusonga mbele hasa katika shughuli za sekta hizi za kilimo. Hongera sana Mheshimiwa.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeshaanza mchakato na ukweli huu unapatikana katika jibu langu la msingi; ukiangalia kwenye mstari wa mwisho, utaratibu wa ndani unaendelea ili kuwasilisha maombi ya fedha Wizara ya Fedha na Mipango. Kwa hiyo, suala hilo la upatikanaji wa hizi Shilingi bilioni 11 tayari utaratibu tumeshauanza na muda wowote tunategemea kupata hizi fedha na tukizipata tutakwenda kufanya kile ambacho Mheshimiwa ameshauri.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kweli tumegundua na utafiti unaonesha kwamba shughuli za kibinadamu zikiwemo za kilimo, mifugo, uvuvi, madini na nyingine, kwa kweli zimekuwa zinaathiri sana vyanzo vya maji, athari ambazo mwisho wa siku zinakwenda kuharibu shughuli za kilimo na kufanya shughuli hizi zisiende vizuri.

Mheshimiwa Spioka, kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba tumeshakaa na tutaendelea kukaa kufanya stadi mbalimbali kwa kushirikiana na wenzetu wa Tawala za Mikoa kwa maana ya wa Halmashauri, Vijiji na wale wa Mamlaka ya Mabonde ili kuona namna ambavyo tunahuisha vyanzo vya maji kwa ajili ya kuboresha shughuli za kilimo.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Pamoja na majibu ya jumla ya Serikali kwenye changamoto hii kwamba imeandaa mwongozo wa usafishaji mchanga, kutoa tope na taka ngumu. Hili ni jukumu ambalo halmashauri yetu ya Manispaa ya Ubungo imeshafanya sana, lakini madhara ni makubwa sana kwenye mto ule, unazidi kupanuka na kuvunja shule na taasisi za Serikali pamoja na makazi ya watu.

Mheshimiwa Spika, inawezekana changamoto hii inahitaji Wizara ya kisekta ingejibu. Naomba niruhusu niulize maswali mawili ya nyongeza, swali la kwanza; je, Serikali itakuwa tayari kujenga kingo imara kwenye Mto wote huo wa Mbezi ili madhara haya yaweze kuondoka?

Mheshimiwa Spika, je, Mheshimiwa Waziri husika atakuwa tayari kwenda nami jimboni ili tuutembelee mto na aone madhara ambayo yametokea kwa wananchi na yatakayotokea kwenye siku zijazo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS (MUUNGANO NA MAZINGIRA): Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Issa Jumanne Mtemvu, Mbunge wa Kibamba, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, moja ya miongoni mwa jukumu letu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira ni kuhakikisha kwamba tunazingatia na tunashughulikia masuala ya vyanzo vya maji ili visiathiriwe na visiathiri wananchi. Niko tayari kufuatana na yeye kwenda kutembea katika Mto Mbezi kuona changamoto hiyo.

Mheshimiwa Spika, kwa swali lake lingine, Ofisi ya Makamu wa Rais, Serikali tuko tayari kuhakikisha kwamba tunajenga huo mradi wa ukuta ambao utatenganisha ili sasa maji yasiweze kuingia huko yakaleta mafuriko. Ila namwomba Mheshimiwa Mbunge yeye kwa kushirikiana na Halmashauri ya Manispaa ya Ubungo, kwanza wafanye tathmini ya ujenzi huo, lakini kingine waandike halafu watuletee Ofisi ya Makamu wa Rais ili tuone namna ambavyo tunaweza tukapata fedha kwa ajili ya kuandaa mradi huo. Nakushukuru.
MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI: Mheshimiwa Spika, naomba nikushukuru kwa kunipa nafasi hii. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, ambayo yamesema kikao chamwisho kilifanyika Agosti, 2021 na katika kikao hicho changamoto 11 kati ya 18 zilipatiwa ufumbuzi.

(a) Je, Serikali inaweza kulitaarifu Bunge sasa mambo hayo ni yapi?

(b) Ni lini Serikali italeta Muswada ili mambo yaya sasa yatambulike kisheria kwamba yapo nje ya changamoto zetu na kila mtu afanye ya kwake?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji, Mbunge wa Jimbo la Mwera, kama iifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika changamoto 25, jumla ya changamoto 28 zimeshapatiwa ufumbuzi, miongoni mwa hizo kama ambavyo umenishauri nitampelekea kwa maandishi ili aweze kuziona. Zipo changamoto kwa mfano kulikuwa kuna hoja ya uvuvi katika Bahari Kuu hii ilishapatiwa ufumbuzi, kulikuwa kuna hoja ya mgawanyo wa mapato ilishapatiwa ufumbuzi. Kulikuwa kuna hoja ya mapato yanayotokana na uhamiaji, hii ilishapatiwa ufumbuzi kwa upande wa Zanzibar, kulikuwa kuna hoja ya ucheleweshaji wa miradi ya maendeleo, kusainiwa kwa mikataba ya miradi ya maendeleo Zanzibar hili limeshapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano kusainiwa kwa mkataba ujenzi wa Hospitali ya Mbiguni Zanzibar, ukarabati wa Hospitali ya Mnazi Mmoja Zanzibar, ujenzi wa barabar ya kutokea Chake, Machomanne, Meli Tano kuelekea kwa Binti Abeid kueleka Wete, yote haya na mengine yalishapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mengine kama ulivyoshauri nitampelekea kwa maandishi.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni kuwa jambo hili la Muungano ni jambo ambalo hati zake zimesainiwa zipo na zina nguvu kisheria. Kwa hiyo, nimuambie tu Mheshimiwa Mbunge, kwa sababu ni jambo ambalo linahitaji ridhaa ya pande zote mbili, wacha tukakae tutakapoona kuna haja ya kuleta kama Muswada basi tutalileta hapa. Nashukuru. (Makofi)
MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa kumekuwa na malalamiko mengi sana kwa Wabunge na baadhi ya wananchi kutokana na ucheleweshwaji na matumizi mabaya ya fedha yanayofanywa na baadhi ya Halmashauri hasa kule Zanzibar: Je, Serikali haioni haja sasa kwa kushirikiana na Serikali ya Zanzibar kubadilisha utaratibu wa fedha hizi, badala ya kupitia Halmashauri sasa kupitia moja kwa moja kwenye account maalumu za Majimbo husika? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili: Kumekuwa na utaratibu usiokuwa rasmi kwa baadhi ya Halmashauri hasa kule Zanzibar, ukizingatia kwamba Jimbo la Nungwi hadi hii leo bado hivi tunavyozungumza hatujapata fedha za mwaka 2021/2022. Hii ni kutokana na hali ya sintofahamu iliyotokezea pale Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini A.

Je, Serikali inawahakikishiaje wananchi wa Jimbo la Nungwi kuhusiana na fedha hizo juu ya upatikanaji wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Sadiki Simai, Mbunge wa wananchi wa Jimbo la Nungwi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo hili la Mfuko wa Jimbo lipo kisheria na limeelezwa kabisa katika Sheria Na. 6 ya mwaka 2012 na katika sheria hii imeeleza wazi kwamba fedha zote za Mfuko wa Jimbo zitakuwa zinapitia kwenye Halmashauri. Sasa kwa kuwa Mheshimiwa ameshauri hilo na kwa kuwa jambo hili lipo kisheria, basi atupe muda tuone namna ya kufanya kwa sababu inabidi twende kwenye sheria ili tuhakikishe kwamba fedha hizi zinakwenda kwenye mifuko ya Wabunge wenyewe. Hata hivyo tulilifanya hili, kwani ilifika wakati tukaona kwamba fedha nyingi zilikuwa zikitumika kinyume na utaratibu. Ndiyo maana Serikali iliamua sasa zipitie kwenye Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la Halmashauri hiyo ama Jimbo lake kwamba mpaka leo fedha zile hazijapatikana na kwa sababu labda zilitumika kwa mambo mengine, tuseme tu kwamba lengo la Mfuko wa Jimbo ni kusaidia kuboresha miradi ya maendeleo katika Majimbo husika na hakuna lengo lingine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hapa tunataka tutoe wito kwa Halmashauri zote, Mabaraza ya Miji yote, kwamba fedha hizi zitumike kwa ajili ya miradi ya maendeleo ya jimbo na siyo vinginevyo. La kwanza, wahakikishe wanawajulisha Wabunge kwamba fedha zimeingia; la pili, wawape fedha hizi kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo lake tutalifutilia na tutahakikisha kwamba fedha zake tutazipata kwa wakati. Nakushukuru.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Changamoto ya Mfuko wa Jimbo kwa upande wa Zanzibar kila siku kila tukija hapa kwenye kikao suala hili linaibuka. Mpaka muda huu nazungumza, mimi Jimbo langu la Chaani sijapokea kwa ukamilifu fedha hizi za Mfuko wa Jimbo. Tumekuwa tukilalamika kila session ya Bunge, bado Serikali hatujaona kuchukua hatua stahiki kwa ajili ya kutatua changamoto hizi ambazo tena tunakubaliana nazo sisi Wabunge kupitia upande wa Zanzibar. Nakushukuru. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Juma Usonge, Mbunge wa Jimbo la Mkwajuni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tukiri kwamba bado kuna changamoto kwenye Mfuko wa Jimbo pamoja na kuboreshwa kwa hizi sheria. Changamoto kubwa tuseme ipo kwenye Mabaraza ya Miji na kwenye Halmashauri. Tulichokipanga baada ya Bunge hili, twende tukakae na viongozi wote wa Mabaraza ya Miji na Wakurugenzi wa Halmashauri wote Zanzibar ili tuwaeleze umuhimu wa fedha hizi kufika kwa wakati kwa Waheshimiwa Wabunge ili waweze kutekeleza miradi yao.
MHE. OMAR ALI OMAR: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa hii ya kuuliza maswali mawili madogo ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la kwanza ni kwamba pamoja na juhudi kubwa za Serikali za kuangalia hifadhi ya mazingira lakini swali la kwanza ni kwamba Serikali ina mpango gani wa kuviwezesha vikundi vinavyojishughulisha na upandaji wa mikoko pamoja na matumbawe?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, katika visiwa vidogovidogo vilivyopo Pemba Kisiwa cha Mtambwi Mkuu ni moja kati ya visiwa ambavyo vinaathirika kwa hali ya juu kabisa.

Je, Serikali ina mpango gani kukihami kisiwa kile ili kisipotee katika sura ya dunia? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA
MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Omar Ali Omar, Mbunge wa Wete, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Omar kwa kazi nzuri anayoifanya kutuwakilisha katika suala zima la utunzaji na uhifadhi wa mazingira hasa katika suala la uhifadhi wa vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zipo juhudi mbalimbali ambazo tumezichukua katika kuhakikisha kwamba tunawasaidia hawa watu wa vikundi, cha kwanza ni kuelimisha. Tumegundua kwamba changamoto kubwa iliyokuwepo ni kwamba watu wengi taaluma kwao imekuwa ni changamoto. Kwa hiyo, tumekuwa tukichukua juhudi ya kuwaelimisha kuhusu suala la uhifadhi wa mazingira pia tunawahamasisha juu ya upandaji wa miti na kuishughulikia, kwa sababu kuipanda ni suala moja na kuishughulikia ni suala jingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nitoe wito kwa jamii hasa Waheshimiwa Wabunge tushirikiane, kila mmoja apande mti lakini kila mtu ashughulikie mti wake, kuipanda tu miti haitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa zaidi kwa kushirikiana na Wizara ya Uvuvi tunahakikisha kwamba tunapambana dhidi ya uvuvi haramu ambao unaharibu hayo masuala ya mazingira.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa Vijiji ambavyo vipo hatarini kutoweka kwa miamba hii ya matumbawe ni Kijiji cha Pwani Mchangani ambacho kipo katika Jimbo langu la Chaani.

Je, ni lini Serikali itachukua hatua za haraka ili sasa kunusuru Matumbawe yale yasiharibike lakini pia yasitoweke kutokana na shughuli za kibinadamu ambazo zinaendelea?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Juma Usonge Mbunge wa Jimbo la Chaani Kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nae nimshukuru na nimpongeze kwamba ni mmoja wa miongoni mwa Mabalozi wetu wazuri wa mazingira hasa katika Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo juhudi mbalimbali ambazo tumepanga kwa ajili ya kuhakikisha kwamba Kijiji cha Pwani Mchangani kinaendelea kuwa salama hasa katika suala zima la uhifadhi wa mazingira. Moja ni kupitia taaluma lakini yapo matumbawe ambayo tumeshayaandaa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunakwenda kuyaweka angalau sasa vile viumbe ambavyo vimo kwenye bahari viweze kuishi katika mazingira ambayo wanaweza waka-survive ili waweze kuhifadhi mazingira zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
MHE. ASKOFU JOSEPHAT M. GWAJIMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Pamoja na majibu mazuri ya Mhehimiwa Waziri nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa kitambulisho cha NIDA kinamthibitisha mtu kwamba ni Mtanzania, inakuwaje sasa wakati mtu anakwenda kutafuta hati ya kusafiria (Passport), anaombwa vitu vilevile alivyokuwa anaombwa wakati anaomba hati ya kusafiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili Je, Serikali haioni sasa umuhimu wa kufanya hiyo namba ya Kitambulisho cha Taifa kuwa hiyo hiyo namba ya TIN na kuwa hiyo hiyo namba ya mita ya umeme kwa watu ambao wana nyumba zao? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali la Mheshimiwa Dkt. Askofu Josephat Gwajima maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapofika wakati tukawa tuna mdadisi mtu mara mbilimbili maana yake tumemdadisi kwenye NIDA pia tunamdadisi tupate maelezo yake kwenye hati ya kusafiria, suala kubwa hapa tunataka tujiridhishe. Kwa hiyo inabidi lazima tufike wakati tumhoji ili tuweze kujiridhisha kwa sababu hali za mifumo zinabadilika lakini na hali za binadamu pia zinabadilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, inawezekana kitambulisho ambacho alikuwa nacho, kwa sababu vitambulisho pia vina-expire date, vinakuwa na date of issue, kwa hiyo tunataka tujiridhishe kwamba ni yeye na labda alipotokea na mazingira mengine, kwa hiyo, kubwa hapa huwa tunataka kujiridhisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lake la pili ameuliza Je, Serikali haioni haja ya kusema sasa tuunganishe mifumo. Hilo ni jambo jema na tunalichukua ni wazo zuri kwenda kulifanyia kazi kwa sababu siyo Tanzania tu, zipo nchi ambazo tayari zimeshafanya huo mfumo na zinatumia NIDA na kitambulisho kingine. (Makofi)
MHE. HAJI AMOUR HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa ruhusa yako nina maswali mawili ya nyongeza: -

Swali la kwanza, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania yupo katika jitihada za kuwaita wawekezaji nchini kwetu Tanzania kwa ajili ya kuja kuwekeza nchini mwetu, wakati huo huo pia kuna kuwa na idadi kubwa ya wageni ambao wanakuja Tanzania kwa ajili ya kuja kujifunza.

Je, kwanini vibali vinachelewa?

Swali la pili, ninamuomba Mheshimiwa Waziri kama ataridhia kwake tukaongozana mimi na yeye kufanya ziara ya maksudi kwenda kuangalia mtambo ule ambao ulikuwepo Zanzibar na kuangalia vile vibali walau 100 vilivyochapishwa kwa mwaka huu 2022. Naomba sana hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Haji Mbunge wa Pangawe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya kuchelewa, kwanza nikiri hii changamoto ipo, lakini changamoto hii inasababishwa zaidi na wananchi wenyewe au wale ambao wanaotaka kuomba vile vibali vyewewe. Sababu moja ni za kimtandao unajua tumeingia katika e-permit kwa hiyo time nyingine inawezekana mtandao ukawa unasumbua ukachelewesha kidogo, lakini sababu nyingine ni kwamba wananchi wenyewe au wale ambao wanaomba zile permit huwa wanafika wakati wanakuwa wanashindwa kukamilisha vigezo na masharti hivi vinapelekea sasa kuchelewa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa ni kwamba kuna baadhi ya watu huwa wanawapitisha hawa wageni katika njia ambazo siyo rasmi wala siyo sahihi hii inapelekea vilevile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine kwa upande wa kwenda kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi tupo tayari kwa ajili ya kwenda huko kukagua huo mtambo huko Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)
MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la kuwapatia Watanzania vitambulisho vya Taifa limechukua muda mrefu sana na imekuwa na sintofahamu. Kuna Watanzania ambao takribani miaka mitatu mpaka minne wana namba tu hawana kadi.

Je, ni nini kauli ya Serikali kuhusiana na jambo hili? Kama mmeshindwa muwaambie Watanzania kwamba mmeshindwa na haiwezekani zoezi hili. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli hili jambo lilikuwa limekwama kidogo, lakini tulikuwa tuna changamoto na sababu ya kwamba hivi vitambulisho vichelewe kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba bado Serikali haijashindwa kuwapatia wananchi vitambulisho, hivi ninavyokuambia vitambulisho vimeshazalishwa na tayari huko Wilayani vimeshasambazwa. Kikubwa ni kwamba kama Wilaya ambavyo vitambulisho havijafika basi tuelezane tujue namna ya kufanya lakini vitambulisho tayari vimeshapelekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, even if vinazalishwa kwa speed siyo ile ya kawaida lakini kwa ufupi ni kwamba vitambulisho vinazalishwa na vitawafikia wananchi ili waweze kupata hiyo huduma ya vitambulisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru. (Makofi)
MHE. ANASTAZIA J. WAMBURA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali madogo mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, hii dust suppression system inapunguza vumbi kwa kiasu kidogo sana, lakini pia ukienda bandarini pale utakuta maji yameshakuwa meusi kutokana na hili vumbi. Swali langu la kwanza: Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba inatunza au inalinda vyanzo vya maji ili kusudi visiweze kuathirika kutokana na yale maji ya mvua yanayotiririka ambayo tayari yameshakuwa na vumbi? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili: Je, Serikali itakuwa tayari kupokea ushauri kwamba haya makaa ya mawe kutoka kwenye migodi yawe yakisafirishwa yakiwa yamefungwa kwenye vifungashio, kwa mfano, labda viroba au maboksi ili kusudi kuzuia lile vumbi lisitimke wakati wa usafirishaji, wakati wa kushusha mzigo na vile vile wakati wa kupakia mzigo katika meli? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba swali la Mheshimiwa Anastazia James Wambura, Mbunge wa Viti Maalum, kutoka Mkoa wa Mtwara, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Usimamizi na Utunzaji wa Vyanzo vya Maji imewaelekeza watu wote, makampuni, taasisi zote zinazofanya shughuli zote ambazo zitakuwa zinagusia sehemu zenye maji au vyanzo vya maji; tumeshawaelekeza pamoja na hawa wa Mtwara wanaofanya biashara hiyo. Kwanza tumewaelekeza kwa kuwapa taaluma, lengo na madhumuni, watunze vyanzo vya maji. Pia tumekuwa tunasimamia sheria kwa kushirikiana na wenzetu wa NEMC, watu wa Halmashauri na wengine. Lengo na madhumuni ni watu watunze vyanzo vya maji.

Mheshimiwa Spika, pia tumeshakaa nao kwa ajili ya kuhakikisha kwamba tunachukua hatua mbalimbali, na tayari zipo hatua ambazo NEMC wamezichukua kwa baadhi ya watu hawa. Hapa nataka nitoe wito kwa Watanzania wote wanaofanya shughuli za kibinadamu karibu na vyanzo vya maji, wahakikishe kwamba wanatunza vyanzo vya maji. Kinyume na hapo, sheria na taratibu zitakuwa zinachukuliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili, tupo tayari, tumepokea huo ushauri. Ingawa makaa ya mawe haya yanakuwa ni mawe makubwa, lakini tutajua namna ya kuwashauri wafanyabiashara wawe wanaweka katika package maalum ili yaweze kupunguza hilo vumbi ambalo linaweza kuathiri afya za wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. DAIMU I. MPAKATE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Suala la makaa ya mawe kutoka Ngaka kupita Songea – Tunduru mpaka Mtwara kuna baadhi ya madereva wamekuwa na tabia ya kusambaza yale makaa ya mawe barabarani, aidha kwa magari kuanguka au kwa kutokufunika. Hii imekuwa ni hatari sana kwa wananchi wanaokaa karibu na barabara hizi. Je, Serikali iatoa kauli gani kwa hawa madereva wanaofanya tabia hii ya kusambaza makaa ya mawe barabarani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Daimu Mpakate, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hii ni changamoto, tumeiona na mara kadhaa tumekuwa tukikaa na wafanyabiashara hawa pamoja na vyombo vingine au taasisi nyingine zinazohusika ili kuwaeleza hawa wafanyabiashara kwamba wasiyatawanye ama wasiyaweke makaa ya mawe haya katika maeneo tofauti, bali wawe na vituo maalum vya kuweka ili kuepusha athari zinazojitokeza zikiwemo hizo za uchafuzi wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendelea kutoa taaluma na kuwaambia wananchi wasiyasambaze haya mwisho wa siku yakawa yanaleta athari. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. FELISTA D. NJAU: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Katika Kata ya Wazo, Mkoa wa Dar es Salaam, kuna Kiwanda cha Twiga Cement ambacho kinatiririsha vumbi jingi kuelekea kwa makazi ya wananchi: Nini mkakati wa Serikali kuwanusuru wananchi hawa kuhakikisha hawapati athari za kiafya? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la moja la nyongeza kutoka kwa Mheshimiwa Felista Njau, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hili jambo tumekuwa tunalipigia kelele sana na hasa hivi viwanda ambavyo vipo karibu na makazi ya wananchi. Tumekuwa tunalisemea sana na tumeshachukua hatua nyingi za kinidhamu lakini pamoja na hayo. tumeshakuwa tunakaa na wamaliki wa viwanda hivi na pia tumekuwa tunawapa taaluma.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba jambo hili tunaendelea kulifanyia kazi ili tuhakikishe kwamba wananchi wanaendelea kuwa salama kutokana na hizi adha na changamoto za viwanda ambazo zinaweza zikawaathiri wananchi kwa njia moja ama nyingine, nakushukuru.
MHE. SULEIMAN HAROUB SULEIMAN: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, pamoja na majawabu mazuri ya Mheshimiwa Naibu Waziri, nina maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza ni lini miradi ambayo inahusiana na mabadiliko ya tabia nchi iliyopo Zanzibar SMT wataimaliza? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la pili, Zanzibar inashirikishwa vipi kwenye mikutano ya Kimataifa hasa inayohusu masuala ya tabia ya nchi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Suleiman, Mbunge Mwakilishi kutoka Baraza la Wawakilishi Zanzibar, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ipo miradi mingi ambayo inatekelezwa ama inasimamaiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na inatekelezwa Zanzibar. Kuna miradi ile ambayo inasimamiwa na Ofisi ya Makamu wa Rais lakini kuna miradi inayosimiamiwa na NEMC. Kwa mfano, kuna Mradi wa Adaptation Fund ambayo ipo Zanzibar na imetekelezwa maeneo tofauti. Hii tayari imeshakamilika na wananchi wameshaanza kunufaika na miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, pia kuna miradi ya EBA ambayo hivi karibuni kama mnakumbuka tuliwahi kukabidhi boti za uvuvi Tumbatu na Mheshimiwa Rais wa Zanzibar, lengo na madhumuni Serikali ya Jamhuri ya Tanzania inaunga mkono juhudi za Uchumi wa Bluu kwa upande wa Zanzibar na suala nzima la uhifadhi na utunzaji wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, vile vile kuna miradi ya LSDF. Hii ni miradi ambayo imekuja kwa ajili ya kukuza kilimo, kuboresha ardhi iliyoathirika na athari za mabadiliko ya tabia nchi. Pia kuna miradi ambayo haijakamilika; hii tumeshatoa maelekezo kwamba ndani ya mwezi huu ianze. Ni mradi wa uchimbaji wa bwawa la maji uliopo Bumbwini Makoba. Tumesema ndani ya mwezi huu uanze na utaanza kwa ajili ya kunufaisha wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili…

SPIKA: Kwa kifupi.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, Zanzibar inapata ushirikiano mkubwa kushirikishwa kutoka Serikali ya Jamhuri katika vikao vinavyohusina na mazingira katika mambo ya Kimataifa. Hivi karibuni tulikuwa tuna kikao cha COP27 Mkutano wa Kimataifa ambapo Zanzibar tulishiriki. Tanzania tulishiriki lakini Zanzibar walileta delegation yao, tulikuwa na Mkurugenzi wa Mazingira na Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha kuonesha kwamba tunao ushirikiano wa karibu baina ya Serikali mbili hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza maswali ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba moja; kwa kuwa tayari kuna jitihada ambazo zilishafanyika toka mwaka 2014 za kuanzisha mfumo wa fedha wa mabdiliko ya tabianchi (Tanzania Climate Financing Mechanism), pamoja na tafiti nyingi pia zilifanyika, ili kuanzisha mfuko wa mabadiliko ya tabia ya nchi.

Je, kwa nini Serikali haioni haja ya kutumia taarifa na tafiti mbalimbali ambazo zilifanyika huko kabla ili kuweza kuharakisha utaratibu huu wa kuanzisha mfuko wa mabadiliko ya tabianchi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba mbili; kama ninavyokumbuka kwamba dunia inalichukulia suala la mabadiliko ya tabianchi ni janga kubwa kuliko athari nyingine za kimazingira;

Je kwa nini Serikali haioni haja ya kutengeneza mfuko wa mabadiliko ya tabia ya nchi unaojitegemea ili kuweza kuchochea ufadhili na kuweza kuhamasisha wafadhili na wahisani kuweza kuchangia mfuko wa mabadiliko ya tabianchi sambamba na zile jitihada za Serikali kuweza kuji- commit fedha zaidi katika huu mfuko? Ahsnate sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Soud Mohammed Jumah, Mbunge wa Jimbo la Donge, maswali mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo alilolishauri Mheshimiwa Mbunge, tayari ni jambo ambalo tumeshaanza kulifanyia kazi. Hivi ninavyokwambia tumeshaanza mchakato wa mapitio ya Sheria hii ya Mazingira ambayo imo katika Sura ya 191. Tumeanza mchakato huu lengo na madhumuni ili kuona, kwanza namna gani mfuko huu utaundwa, lakini vipi unaweza ukapokea fedha, namna utakavyozitoa hizo fecha, ni fursa na faida gani na ni athari zipi ambazo zinanweza zikapatiwa msaada ama zikasaidiwa kupitia mfuko huu, baada ya mfuko huu kwa sasa unaanza kutoa hizo. Kwa hiyo kikubwa nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba mchakato umeanza na muda wowote unaweza ukakamilika na hiyo hali ikaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kingine nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge, kwamba lengo na adhma ya Serikali katika kuunda mfuko huu kwanza ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unajitegemea, lakini la pili ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unapata fedha ya kutosha, tatu ni kuhakikisha kwamba mfuko huu unapata misaada kutoka kwa wafadhili mbalimbali, ili lengo na madhumuni mfuko huu uweze kusaidia wananchi katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi na utunzaji na uhifadhi wa mazingira. Hivyo nimwambie tu Mhehsimiwa Mbunge kuwa adhma ya Serikali inaendanana na mawazo yake.

Mheshimiwa Mwenyekti, nakushukuru.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafsi. Kwa kuwa mabadiliko ya tabianchi yana madhara makubwa na huweza kusababisha majanga.

Je Serikali inaimarishaje kuwapa taaluma kisasa zaidi ya uokozi na uhifadhi watu wengi zaidi badala ya kutegemea JWTZ na Zima Moto pekee?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO
NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha Abdullah Juma, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Zanzibar, najibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, athari za mabadiliko ya tabianchi siku zote zinasababishwa na zinachangiwa kiasi kikubwa na shughuli za kibinandamu ambazo binadamu wanafanya katika maisha yao ya kila siku. Zikiwemo shughuli za ukataji wa miti, shughuli za uharibifu wa vyanzo vya maji, shughuli za uchomaji wa misitu, shughuli za ufanyaji wa shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya hifadhi na shughuli nyingine. Kwa hiyo hatua moja ambayo tumeichukua kwanza ni kuwaelemisha wananchi, kuwaeleza athari ambazo zinapatikana baada ya wao kufanya hizo shughuli za kiubinadamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili amabalo tunalifanya ni kusimamia sheria. Kwa sababu mbali na kuwaelimisha lakini kwa vile sheria zipo ni kuzisimamia sheria. Tatu ni kuchukua hatua za kisheria kwa wale wote wanaochafua ili lengo na madhumnuni tusiwape mzigo wengine wakina Zima Moto na watu wanaoshirikiana maafa na watu wengine.

Mhehsimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Pamoja na jitihada nzuri za Serikali ambazo wiki iliyopita tuliona imetoa kanuni na miongozo ya namna gani Taifa litanufaika na namna ya kuuza ile hewa ya ukaa, kwa maana ya Carbon emission.

Je, Ofisi ya Makamu wa Rais Mazingira iko tayari kutoa mafunzo kwenye Halmashauri ambazo zimekuwa mstari wa mbele katika kupanda miti kama ilivyo Halmashauri ya Mafinga, Mufindi, Kilolo na Halmashauri katika Mkoa wa Njombe?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Chungahela kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefika wakati tumeona kwamba jambo hili la biashara hii ya hewa ukaa ni jambo ambalo pamoja na kwamba lina umaarufu lakini bado lina ugeni kwa baadhi ya maeneo katika nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kikubwa ambacho tumekifanya kwanza tumeandaa kanuni. Tayari kanuni zipo na katika kanuni zile tayari imeelezwa namna ambavyo tutapita kila kijiji na kila eneo. Hivi tunavyokwambia tayari tumeshashirikiana na Wizara nyingine za kisekta wakiwemo watu wa Halmashauri na Wizara nyingine ili lengo na madhumuni kupitia maeneo yote ya Tanzania hasa kwa upande huo; ili lengo na madhumuni kuwaeleza wananchi fursa na faida zinazopatikana katika biashara ile ikiwa ina mnasaba wa kutunza na kuhifadhi mazingira. Kwa hiyo nimuhakikishie
Mheshimiwa Mbunge katika maeneo aliyoyataja yote tutapita, tutatoa elimu, tutawaelimisha wananchi ili waweze kujua fursa na faida zinazopatikana katika biashara hii ya carbon credit.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na ninamshukuru sana Naibu Waziri kwa majibu mazuri. Nina swali moja la nyongeza.

Kwa kuwa, biashara hii huwa inahusisha upandaji na utunzaji wa miti. Je, Serikali haioni umuhimu wa kusukuma hii biashara iende katika maeneo ya Kilimanjaro inayopakana na Mlima Kilimanjaro ili kwanza tutunze ule msitu ili Mlima usiharibike na wananchi wa Kilimanjaro wajipatie kipato?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Profesa Patrick Ndakidemi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nikiri na niseme kwamba ipo haja ya mradi huu kwenda Kilimanjaro kwa lengo na madhumuni ya kuhifadhi na kutunza mazingira.

Mheshimiwa Spika, pia kuna haja ya mradi huu kupelekwa Kilimanjaro na tutakwenda kuhakikisha tunapeleka ili lengo na madhumuni wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro na vijiji vilivyomo ndani ya Mkoa huo waweze kunufaika, kwa sababu mradi huu si kwamba tu unanufaisha Serikali Kuu lakini hata vijiji vidogo vidogo vinanufaika kupitia mradi huu, kwa sababu kuna asilimia maalum huwa inapangwa kwenye mradi huu.

Mheshimiwa Spika, tayari tumesha-practice katika Mkoa wa Katavi, Manyara na Mikoa mingine. Tumeona tayari zipo shule, yapo maji safi, zipo zahanati zilizojengwa kutokana na asilimia ya mradi huu. Ninakushukuru. (Makofi)
MHE. JUSTIN L. NYAMOGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kuniruhusu kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Spika, katika Wilaya ya Kilolo yupo mwekezaji anaitwa Udzungwa Corridor na tayari anapanda mashamba makubwa ya miti kwa ajili ya biashara hiyo. Kwenye vivjiji vinavyozunguka kuna misitu mingi ya asili inayofanana na hiyo hiyo inayopandwa.

Je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuhakikisha ile misitu ambayo wanavijiji wameitunza na yenyewe inaingia kwenye huo mfumo wa biashara badala ya kutegemea tu ile ambayo Mwekezaji anawekeza na anapanda miti ile ile? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lazaro Nyamonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza katika kitu ambacho tunakithamini sana ni upandaji wa miti. Pili tunashughulika na suala zima la kuishughulikia miti. Kwa hiyo, kikubwa nimwambie misitu yote ya asili kama ambavyo nimeeleza katika jibu la msingi kwamba sasa hivi Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, kwa kushirikiana na Wizara ya Maliasili na Utalii, tumeshaandaa muongozo wa usimamizi wa misitu yote ili lengo na madhumuni tuingize kwenye mpango huo pia tuweze kunufaisha vijiji vilivyozunguka na pia tunufaishe Serikali, pia tutunze na tuhifadhi mazingira. Ninakushukuru. (Makofi)
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Kama tunavyotambua huu mradi wa uvunaji wa hewa ya ukaa ni muhimu sana kwa Taifa letu, inasaidia kupunguza masuala mengi ambayo yanasababishwa na uchafuzi wa kimazingira.

Mheshimiwa Spika, swali langu, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia akinamama ambao wamejitolea kwa makusudi kupanda miti ya mikoko Zanzibar katika Vijiji vya Bwimbwini, Bweleo na maeneo mengine na hawa wanawake wanapata changamoto mbalimbali kuhusu kupata miti na mambo mengine ili ile miti kuweza kustawi vizuri. Je, Serikali ina mpango gani wa kuwasaidia akinamama hawa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, asante. Naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Asya, Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Asya amekuwa mmoja wa miongoni mwa vinara ambao wanapambana na suala zima la uhifadhi wa mazingira katika Mkoa wa Kaskazini. Kikubwa tuna mikakati mingi ya kuhakikisha kwamba tunawasaidia akinamama kwa sababu tumegundua kwamba ni moja ya miongoni mwa vinara wazuri wa uhifadhi wa mazingira na kupambana dhidi ya mabadiliko ya tabia ya nchi.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, kuwapa elimu kwa sababu tumegundua kwamba akinamama wengi wana juhudi, wana jitihada na wana hamu ya kuhifadhi mazingira, lakini tumegundua utaalam kidogo umepungua, kwa hiyo tunawapa taaluma.

Mheshimiwa Spika, la pili, tumefikiria pia kuona namna ya kuwasaidia kuweza kupata mitaji ili lengo na madhumuni yaweze kufanya hizo kazi zao za uhifadhi wa mazingira vizuri. Nakushukuru.
MHE. AGNESTA L. KAIZA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi ili niweze kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Mradi huu umechukua muda mrefu kutekelezwa na majibu ya Serikali muda wote yamekuwa ni haya; na kipindi kutoka sasa hadi Julai, ambapo Mheshimiwa Waziri amesema mradi huu utakuwa umetekelezwa ni takribani miezi mitatu tu. Sasa swali langu, Mheshimiwa Waziri analihakikishia Bunge hili Tukufu kwamba kufikia kipindi hicho, taratibu zote ikiwa ni pamoja na kulipa fidia wananchi watakaoguswa na mradi zitakuwa zimekamilika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; Bonde la Mto Msimbazi ni chanzo kikuu cha mafuriko katika barabara iendayo Kariakoo eneo la Jangwani. Barabara hii inaelekea katika kitovu cha uchumi wa nchi. Sasa, swali langu kwa Serikali;

Je, ni mkakati gani wa dharura umeandaliwa kwa kipindi hiki ambacho mvua zinaendelea kwa kasi katika Jiji la Dar es Salaam?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Mbunge, wa Viti Maalum, Mheshimiwa Agnesta Lambert Kaiza, maswali yake mawili ya nyongeza kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunapotaka kufanya jambo lolote, hasa jambo ambalo limezunguka kwenye maeneo ya makazi ya watu si kwamba tu tunaangalia kwenye fidia lakini kuna baadhi ya mambo ya msingi huwa tunaangalia. Kwanza katika mazingira kuna kitu kinaitwa EIA, Environment Impact Assessment; kwa hiyo kwanza tunaziangalia athari za kimazingira. Je, tutakapofanya hilo jambo tunaweza tukawaathiri vipi wananchi kwenye hilo. Lakini pia kuna kitu tunakiita PA property assessment, kwamba je, mali za wananchi wanavipando vyao, wana nyumba zao wana makazi mengine.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa ufupi ni kwamba hili jambo tumeshalikali kitako na tayari tathmini inaendelea ni mtoe hofu Mheshimiwa, tunalithibitishia Bunge hili pamoja na hizo tathmini ambazo ambazo zinaendelea lakini bado tunaendelea na kama tulivyoeleza kwamba miezi michache inayofuata ujenzi huu unaanza.

Mheshimiwa Spika, lakini je, tunajuhudi au jitihada gani katika kuzuia mafuriko; nimwambie tu kwamba tumeshakaa pamoja, sisi Ofisi ya Makamu wa Rais, pamoja na maafisa wetu wa mazingira tumekaa na halmashauri tumekaa watu wa TARURA, tumekaa na watu wengine ili kuona namna ambavyo tunaweza tukapunguza angalau hizo athari za mafuriko, zikiwepo za kutengeneza vi-streams vidogovidogo vitakavyoyaondosha maji pale na kuyapeleka maeneo ya bahari ili pale yasituwame na yakapunguza athari kwa wananchi. Nakushukuru.
MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu yake mahiri kabisa kwamba ninaamini kabisa kwamba anafahamu changamoto hizi zilivyo. Kwa kuwa mradi huu wa Bonde la Mto Msimbazi ni hoja kuu ya Jimbo la Kinondoni, na kwa kuwa sasa Serikali inakwenda kuanza mradi huu Julai, 2022. Je, Serikali iko tayari sasa kutoa mpango wa utekelezaji, kwa maana ya program and planning of action, ili wananchi wale wa mto Msimbazi waweze wakajua ni lini wanatakiwa wanaondoke na ni lini kabisa watatakiwa waweze kupata fidia zao pale itakapobidi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimba Abbas, Mbunge wa Jimbo la Kinondoni, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Abbas kwa kuwa Jimbo lake na yeye ni moja ya miongoni mwa Majimbo yaliyopita katika Mto Msimbazi lakini anafanya kazi kubwa ya kutusaidia kama Serikali kwa kuwaelewesha wananchi. Namwambia Mheshimiwa Tarimba Abbas kwamba aende akawaambie wananchi kwamba tathmini inaendelea. Imeshaanza kama miezi mitatu iliyopita na kwa kuwa inaendelea matokeo lazima wananchi tutawaambia. Kwa hiy,o naomba akawaambie wananchi wa Kata za Kinondoni, Kata za Mzimuni, Kata ya Magomeni, Kata ya Kigogo na maeneo mengine yaliyopita mto huu kwamba tathmini itakapotoka majibu watapewa na lazima tuwaambie kabla ili tusije tukawavamia tukaja tukatengeneza mivutano baina ya wananchi na Serikali. Nakushukuru.(Makofi)
MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana na mimi kuweza kunipa nafasi hii kuuliza swali dogo la nyongeza.

Je, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina mpango gani wa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar juu ya kuandaa mradi utakaoenda kuzuia maji ya bahari kuendelea kumeza kingo kule maeneo ya Nungwi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Simai, Mbunge na mtumishi wa wananchi wa Jimbo la Nungwi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali inayompango ama ilishakuwa na huo mpango na ndiyo maana tayari kuna baadhi ya kingo kwa upande wa Zanzibar ambazo tayari zimeshajengwa na hii ni kutokana na athari kubwa ya kimazingira ambayo ilifika wakati maji ya bahari yanaingia kwenye vipando vya wananchi ikiwemo mihogo, migomba ambayo haihimili maji ya chumvi. Pia maji haya yalikuwa yanaingia kwenye maeneo ya makazi. Serikali kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakaona kuna haja ya kushirikiana katika suala hili. Tayari yako baadhi ya maeneo kwa mfano Kisiwa cha Pemba maeneo ya Wete, Micheweni na maeneo ya Unguja pia tumeanza. Namwambia Mheshimiwa kwamba katika bajeti ambayo tumeisoma juzi tutajitahidi tutenge fungu kwa ajili ya kulipa kipaumbele Jimbo lako kwa ajili ya kujenga hizo kuta. Nakushukuru.
MHE. PROF. KITILA A. MKUMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, Wananchi wa Jimbo la Ubungo wameathirika sana na mafuriko ya mito Gide, Mto China na Mto Ng’ombe, ninavyoongea Mtaa wa Kibangu leo nyumba za wananchi 12 zimebomolewa na mto huo. Nauliza kwa nini Serikali isichukue hatua za dharula za kujenga gambiozi katika mito hiyo ili kuokoa maisha ya wananchi wakati tunasubiri mradi huo? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge Profesa Kitila kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imefika wakati na imeona athari ambazo zinajitokeza hasa zinazosababishwa na mito hii mikubwa na hasa kipindi cha mvua kubwa kama hiki ambacho tukonacho. Namwambia Mheshimiwa Profesa kwamba wazo na fikra alilolitoa ni jambo ambalo tayari tumeshakaa na tumeshalifikiria, lakini kwa heshima ya wazo lake tunalichukua na tunazidi kwenda kulifanyia kazi. Nakushukuru.
MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kuniona. Kwa kuwa ndani ya Jimbo la Kibamba kuna Mto Mbezi na Mto Mpiji ambao kwa muda mrefu wananchi wamedhurika sana na mafuriko, nyumba zao lakini pia na taasisi kama shule zimekuwa zikiondoka.

Je, Serikali ina mkakati gani sasa kukabiliana na hali hiyo katika mito hiyo miwili Mto Mbezi na Mto Mpiji?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mtemvu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tunayo mikakati mingi kwa sababu tunafahamu athari za kimazingira zinazosababishwa na mito hii ni athari kubwa. Mwisho wa siku zinaharibu vipando, zinaharibu makazi lakini pia zinaweza kuleta hata maradhi kwa sababu maji yakija yanakuja na takataka, yakirudi yanarudi maji peke yake takataka zinabakia kwa hiyo tunajua hata maradhi yanatokea. Kwa hiyo iko mikakati mingi kama Serikali ambayo tumeamua kuifanya, ikiwemo kwanza kuhakikisha kwamba tunajenga hizo kingo lakini pia tunasaidia katika kuwaelimisha wananchi namna ambavyo wanaweza wakapunguza hizo athari na wakaepukana na hizo athari zinazosababishwa na mito hii. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi niulize maswali madogo ya nyongeza. Ninamshukuru Mheshimiwa Waziri kwa majibu yake mazuri

Mheshimiwa Mwenyekiti, kumekuwa kuna vikundi ambavyo vimekuwa vikijishughulisha na utunzaji wa mazingira na yeye mwenyewe amekiri hata wanafunzi wameendelea kufungua program zao. Changamoto kubwa vikundi hivi vinakuwa vina ukosefu wa fedha ili viweze kufanya vizuri zaidi.

Je, Serikali inawasaidiaje, vikundi hivi viendelee kupanda miti mingi na kuendelea kutunza mazingira ambayo wanayaishi?

Swali la pili, ili kupunguza shughuli za kibinadamu kuzunguka milima na vyanzo vya maji.

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwezesha kufanya shughuli zingine kama za ufugaji, uvuvi, katika maeneo ambayo wanazunguka wananchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS - MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa Dkt. Ritta Kabati kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatambua uwepo wa vikundi mbalimbali ambavyo vinahitaji kusaidiwa, lakini tunajiridhisha na kuangalia umuhimu wa vikundi hivyo na kwa kiasi gani wanasaidia na wao katika kuimarisha mazingira ndani ya milima lakini na vyanzo vya maji. Serikali ipo tayari kabisa kuwasaidia vikundi hivyo kwa ajili ya kuimarisha mazingira yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali lake la pili, namna gani tutawezesha, tutawezesha kwa kuwapatia taaluma mbalimbali na kuwaita katika mikutano yetu ili kuwapa taaluma kwa ajili ya kuimarisha mazingira ndani ya nchi yetu.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Tatizo lililo kwenye milima ya Iringa linafanana kabisa na tatizo lililoko tambarare ya Mlima wa Kilimanjaro kwa ajili ya mabadiliko ya tabia nchi. Je, Serikali itaungana lini na wanawake wa Mkoa wa Kilimanjaro, ambao wako tayari sana kurejesha uoto huo kwa kuotesha miti katika vihamba vyao, hususani miti ya matunda? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS - MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lake ni kweli tunajua kwamba wanawake ama vikundi mbalimbali wakiwemo wanawake, wanaimarisha sana suala la mazingira kwa upandaji miti, pamoja na na miti ya matunda. Serikali inaahidi kutoa motisha kwa wale ambao watafanya vizuri kwenye kampeni yetu kapambe ambayo itamalizika tarehe 30 Juni.
MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa kuwa uharibifu huu unaofanyika kwenye milima, uko vilevile kwenye fukwe za bahari na zile sehemu ambazo bahari inaungana na mito. Mikoko inazidi kukatwa, kila kukicha na hivyo kuharibu mazingira na sehemu za kuzalia viumbe vya majini.

Je, Serikali sasa itakuja na program gani ya kuongeza hamasa katika kupanda mikoko katika sehemu hizo ili kunusuru mazingira hayo.(Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS - MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Asha maarufu kwa jina la ‘Mshua’ kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ina mpango mkakati ambao wananchi wote ambao wanasaidia kupanda mikoko kando kando ya bahari, wanakuwa na taaluma maalum lakini wanapewa motisha. Kwa mfano, Bagamoyo, Zanzibar, ziko sehemu ambazo tayari wameshapanda mikoko na wale ambao wamepanda mikoko well na ikawa inahuika, basi Serikali tunawapa motisha na kufuatilia siku hadi siku. (Makofi)
MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri katika Wilaya ya Rungwe kuna sehemu ya chanzo cha maji cha Kijungu ambayo inapeleka kwenye daraja la Mungu maji yanayoenda kwenye Mto wa Kiwira. Serikali imeacha kwa muda mrefu sana kuweka mazingira na kuhakikisha chanzo hiki kinakuwa salama na kuendelea kuwa historia ya Wilaya ya Rungwe.

Je, ni lini mtapeleka fedha na kuhakikisha mnalinda eneo lile linakuwa salama na linaendelea kuwa kivutio kwa Watanzania na wageni wanaokuja pale?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS - MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu la Mheshimiwa Sophia kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti ambayo imewekwa ya ofisi yetu basi sehemu hii ambayo umeitaja Mheshimiwa tumeichukua na ndani ya bajeti yetu ipo na tutatekeleza mara baada tu ya kikao hiki cha bajeti. (Makofi)
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa vile Mheshimiwa Waziri amekiri kabisa kwamba katika miradi hiyo kuna changamoto ya ucheleweshwaji; naiomba sana Serikali, kama itaridhia.

Kwa nini kwa mwaka wa fedha huu isikamilishe miradi hii kwa kutumia fedha za ndani badala ya kusubiria fedha za wahisani, ambapo hadi leo hii ni muda wa miaka mitano miradi ile haijakamilika?

Mheshimiwa Spika, swali langu la pili; je, Mheshimiwa Waziri yuko tayari kufuatana nami kwenda kuiona miradi hiyo inayotelelezwa kwenye wilaya mbili ilivyosimama na bado hatma ya kukamilika miradi hiyo haijulikani? (Makofi)
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Juma Usonge Hamad, Mbunge wa Chaani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, miradi hii ambayo inatekelezwa Zanzibar, takribani ukiangalia miradi yote; ile ya EBARR na hii ya LDFS ni miradi ambayo kwanza fedha zake zipo, lakini ni miradi ambayo ukiiangalia muda wake wa kukamilika bado yaani haujafika, kwa sababu miradi hii ukamilikaji wake ni mpaka 2024.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Usonge kwamba pamoja na kwamba miradi hii ina fedha za wahisani, lakini pia kuna fedha ambazo zinatoka kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zinakwenda kukamilisha miradi hii. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa asiwe na hofu.

Mheshimiwa Spika, suala la kufatana naye kwenda kukagua miradi hii, nimwambie tu kwamba niko tayari, kama ambavyo nimeshaanza mara ya kwanza, tutakwenda naye kukagua miradi hii na kuona ukamilifu wake na namna ambavyo inanufaisha wananchi. Nakushukuru.
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante, hali ya Mlima wa Kilimanjaro ni mbaya sana. Swali la kwanza kwa kuwa Serikali inakusanya fedha nyingi kutokana na Mlima Kilimanjaro, ni lini Serikali itatenga fungu maalum kwa ajili ya utafiti huo aliousema na pia operation maalum ya kupanda miti katika Jimbo la Hai?

Mheshimiwa Spika, la pili, mara kadhaa nimekuwa nikiomba Fedha za CSR na sijapata majibu humu ndani. Je, Serikali haioni ipo haja ya Wizara hizi mbili ya Muungano na Mazingira pamoja na Utalii kukaa kwa pamoja na kutengeneza mkakati kwa kuhakikisha tunaondoa tatizo la mabadiliko ya tabia nchi katika Mlima Kilimanjaro? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, napenda kujibu maswali mawili ya nyongenza ya Mheshimiwa Saasisha Elinikyo Mafuwe, Mbunge wa Hai, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba tupo tayari kutenga hilo fungu lakini n kiukweli miti mingi hapa katikati ilikufa kutokana na hali ya joto, kutokana na miti kuchomwa hovyo na kukatwa hovyo. Ofisi ya Makamu Wa Rais, Muungano na Mazingira, tayari tumeshakaa kwa kushirikiana na halmashauri na taasisi za kifedha zikiwemo CRDB, NMB na kwa kushirikiana na TFS tayari tumeshaanza huo mchakato wa upandaji miti.

Mheshimiwa Spika, nimwambie pia tuna kampeni yetu ya kusoma na mti ambapo tunashirikisha wanafunzi wa awali, msingi, sekondari, vyuo na vyuo vikuu, tunawahamasisha wapande miti. Jitihada zote tulizozichukua zitafika Kilimanjaro zitafika Hai na miti itapandwa na mazingira tutayatunza.

Mheshimiwa Spika, swali la pili nimwambie kwamba tumekuwa mara kadhaa tumekuwa na Wizara ya Maliasili kwa sababu tunaamini kwamba wao ndio wenye miti kupitia TFS ya kuweza kupanda. Sisi tupo tayari kupanda miti Kilimanjaro. Lakini tumwambie tu Mheshimiwa Mbunge yeye sasa aanze kuchukuwa juhudi ya kuanzisha hiyo Kampeni, halafu sisi kwa kushirikiana na wadau wengine tutakuja tuje tuifanye Kilimanjaro iwe ya kijani na kuhakikisha kwamba miti inapandwa na mazingira yanatunzwa.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kunipa fursa. Wananchi wanaoishi katika vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro hushindwa kuripoti changamoto za kiusalama kule mlimani kama kukata miti na moto kutokana na uhaba au uhafifu wa mawasiliano. Je, Serikali ina mpango gani kusaidia kuboresha mawasiliano katika vijiji vinavyozunguka Mlima Kilimanjaro?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali moja la nyongeza la Mheshimiwa Profesa Ndakidemi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, hii changamoto kweli tumeiona, sometimes unafika wakati kunatokezea majanga ya moto na mambo mengine, wananchi wanashindwa kuweza kutoa taarifa na sisi kama Serikali tukachukua hatua kwa wakati. Nimuambie tu Mheshimiwa kwamba hili jambo tunalichukua na tunakwenda kulifanyia kazi ili matukio yakitokea tuhakikishe kwamba sisi yanatuletea taarifa mapema na tunayachukulia hatua zinazofaa kwa mujibu yaani kwa wakati unaohusika.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. JEREMIAH M. AMSABI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naishukuru Serikali kwa majibu mazuri. Hata hivyo, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la kwanza: Vijiji vya Borenga, Nyiboko, Buchanchali, Nyasulimunti na Gantamome ambavyo vipo kando kando ya Mto Mara kwa muda mrefu sasa vimeendelea kupata adha kubwa na hasara ya mafuriko katika mashamba, na tunaona mpango huu wa Serikali wa miaka kumi: Je, ni lini mpango huu utaanza ili kuondoa hadha hii inayoendelea katika maeneo hayo?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kumekuwepo na mpango mzuri na maarufu kabisa wa Serikali uliojulikana kama Nile Basin Initiative ambao unahusisha maeneo haya ya Mto Mara kujengewa mabwawa makubwa, scheme za umwagiliaji na kudhibiti mafuriko haya: Je, mpango huu sasa wenyewe umefikia wapi? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jeremiah Amsabi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika Serikali hasa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira tunayo nia ya kuhakikisha kwamba tunafanya huo mradi ambao Mheshimiwa ameupendekeza ama ameutaja. Kikubwa nimwambie Mheshimiwa awe na subira kwa sababu miradi hii kwanza lazima tufanye utafiti, tuone namna itakavyowezekana lakini lazima kuna Wizara tukae, kwa sababu kama tunavyoona hili jambo lina Wizara za kisekta lazima tukae Wizara ya Maji, tukae Wizara ya masuala ya Kilimo pia na sisi tukae pamoja, lakini kubwa zaidi atupe muda kidogo tutafute fedha kwa ajili ya kurekebisha ama kukamilisha mradi huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili nimwambie kwamba Wizara hii ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira tumekuwa tuna utaratibu wa kutembelea miradi takribani yote ambayo inasimamiwa na Ofisi yetu. Kila tunapokwenda tunatoa maelekezo kwamba kwanza miradi ikamilike kwa wakati, pili, miradi iwe ya kiwango, lakini tatu, miradi hii ihakikishe kwamba inanufaisha walengwa. Nimwambie tu kwamba miradi yote iliyo katika eneo lake ama jimbo lake tutaifuatilia na tutatoa maelekezo na itakamilika kwa wakati, nakushukuru.
MHE. DKT. DAVID M. DAVID: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa kunipa nafasi. Naomba kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Swali la kwanza; kero za Muungano zimechukua muda mrefu sana na sasa hivi tuko Awamu ya Sita lakini bado kuna kero na zingine mpya zinajitokeza. Ningependa kuuliza ni mambo gani ambayo yanakwamisha kukamilika kwa kero zote za Muungano?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili; Sheria Mama ni Katiba na katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania suala la uchimbaji na utafutaji wa mafuta na gesi vimeorodheshwa kama masuala ya Muungano na jibu la Serikali linaonesha kwamba changamoto hii imemalizika. Je, suala hili kwenye Katiba ya Jamhuri ya Muungano limefutwa kwa sheria gani?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa David Mathayo, Mbunge wa Same Magharibi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimwambie Mbunge na Watanzania kwa ujumla kwamba suala la utatuzi wa changamoto za Muungano halijakwama wala halijasuasua, ni suala ambalo linakwenda kwa sababu mpaka hivi tunavyozungumza asilimia ya changamoto zilizotatuliwa ni nyingi tofauti na zilivyokuwa. Vile vile, katika orodha ya mambo yaliyotatuliwa yapo mengi, tulikuwa tuna changamoto nyingi, lakini sasa hivi kama atarejea kwenye jibu langu la msingi jumla ya changamoto 22 zimekwishatatuliwa. Zilizobakia ni changamoto ambazo Kamati zinazohusika ziko mbioni na zinakaa kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto hizi na Muungano huu uendelee kudumu kama kawaida.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa swali la pili, ni kweli kwamba suala la utafutaji na uchimbaji wa gesi asilia lilikuwa ni changamoto, ilifika wakati lilikuwa Iina mvutano kidogo, lakini kwa sababu ya busara ya viongozi wetu wanaosimamia Muungano huu na Kamati zilizoundwa zikiwemo Kamati za Makatibu Wakuu, Kamati za Wataalam na Kamati zile za Mawaziri, zimefikia mahali pazuri katika kulitatua jambo hili, tena limetatuliwa kwa mujibu wa sheria na taratibu zote na sasa hivi tayari Zanzibar iko vizuri na Muungano unakwenda vizuri katika suala hili la mafuta na gesi.(Makofi)
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kuna msemo wa kisheria unasema, kwa tafsri yangu mimi, haki inayocheleweshwa ni haki inayonyimwa. Kwa kuwa mfuko wa pamoja wa fedha ni takwa la kisheria na ni muda mrefu sasa jambo hili linapigiwa makelele haujaundwa;

a) Je, ni nini commitment ya Serikali juu ya kuundwa kwa mfuko huu?

b) Je, ni lini Zanzibar itapata mgao wake wa hisa wa iliyokuwa East African Currency Board na faida katika Benki Kuu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO
NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu masuala mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khalifa Mohamed Issa Mbunge wa Jimbo la Mtambwe. Kwanza nataka nichukue fursa hii nimpongeze sana Mheshimiwa Khalifa amekuwa ni mfatiliaji mzuri wa masuala haya ya Muungano ambayo yanagusa mustakabali wa nchi zetu zote mbili. Mheshimiwa Khalifa hongera sana kwa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba moja miongoni mwa mambo ambayo hayajapatiwa ufumbuzi kama sehemu ya changamoto ni hili jambo la uundwaji wa hii kamati au Tume hii ya Pamoja ya Fedha. Tume hii ilikuwepo bahati nzuri imekwisha muda wake. Hata hivyo, sisi tayari tumeshapeleka mapendekezo kwa ajili ya kuteuliwa kwa tume hii. Nimwombe tu Mheshimiwa Khalifa awe na subra ili sasa tuzipe mamlaka zinazohusika zifanye uteuzi wa tume hii ili lengo na madhumuni sasa mambo haya ya muungano yaweze kwenda vizuri kama ambavo yanatakiwa kwenda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo nimejibu swali la msingi kwa upande wa swali la pili; ni kwamba changamoto hizi zilikuwa ziko nyingi, lakini kupitia Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Hassan tumefanya juhudi kubwa kupitia kamati zilizoundwa za pande zote mbili. Kwa hiyo nimwambie tu kwamba huu mgawanyo ambao ameuzungumza unakwenda kupatiwa ufumbuzi na tutahakikisha kwamba tunafanya moja miongoni mwa jambo muhimu la utatuzi wa hii changamoto kwenye changamoto ama miongoni mwa haya mambo ya muungano.
MHE. ASIA A. HALAMGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa kero za Muungano, ingawa Mheshimiwa Waziri hapa amejibu, anasema kwamba kero ya bandari imetatuliwa; lakini hadi jana nimepokea simu kutoka kwa wananchi ambao wamesafiri kutoka Zanzibar wamekuja Dar es Salaam na wamezuiwa mizigo yao midogo midogo bandarini. Nataka kujua, Serikali ituambie hapa;

Je, ni lini watalikomesha jambo hili na kero hii kuisha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO
NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu suala la nyongeza la Mheshimiwa Asia Mbunge wa Viti Maalum kutoka Mkoa wa Kaskazini Unguja kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika kikao chetu ambacho tulikaa tarehe 6 Disemba, 2022, miongoni mwa maazimio ambayo tuliazimia, kwa sababu kama nilivyosema kwamba suala la utatuzi wa changamoto za Muungano limeundiwa Kamati Maalum, kuna Kamati ya Wataalam, kuna Kamati ya Makatibu Wakuu lakini kuna Kamati ya Mawaziri. Kwa hiyo, mpaka tarehe hii tulipokaa tulikubaliana na tukatoa maelekezo kwa TRA na ZRA na Wizara zinazohusika kulifanyia kazi suala hili na kutoa mapendekezo ya ni kipi kinatakiwa kilipiwe na kipi ambacho hakitakiwi kilipiwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge aendelee kuwa na subira, hili jambo tunalifuatilia na tunahisi tunapokwenda kwenye kikao kijacho tutalipatia ufumbuzi. Nawaomba Watanzania waendelee kuwa na subira, Serikali zote mbili zinazifanyia kazi hizi changamoto za Muungano.
MHE. AMEIR ABDALLAH AMEIR: Mheshimiwa Spika,ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri ningeomba kuuliza masuala mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa tuna maeneo ambayo yana vielelezo vya kihistoria kati ya Tanzania bara na Tanzania visiwani yanayo shabihiana; kwa mfano hatuwezi kuzungumza biashara ya utumwa tukaielezea sehemu moja ina elezeka sehemu zote mbili wanahistoria Dkt. Livingstone.

a) Je, Wizara yako sasa inaampango gani wa kuyahuisha maeneo haya yenye vielelezo vya kihistoria vinavyotegemeana ili sasa kuusaidia utalii wetu wa ndani kukua zaidi kimapato?

Mheshimiwa Spika, kutokana na mtikisiko wa Uviko 19 tumeona kwamba utalii wetu wa ndani kidogo uliyumba;

b) Je, Wizara sasa ina mpango gani wa mikakati mipya na imara ukiachia mbali hii ya kawaida unayoelezea ya kuweza sasa kuufanya utalii wetu wa ndani uweze kujitegemea angalau kwa asilimia hamsini kwa hamsini, huku ukizingatia kwamba tunapoboresha vya kutosha Tanzania kutokana na ongezeka la watu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Ameir Abdallah Ameir, Mbunge kutoka Baraza la Wawakilishi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ipo mikakati kabambe ambayo imeshaandaliwa na Serikali kuhakikisha kwamba tunaendelea kutunza maeneo haya ya kihistoria. Moja ni kuhakikisha kwamba tunaendelea kuyatunza maeneo hayo yenyewe ili lengo na madhumuni sasa tuweze kuvutia watalii wengi; lakini cha pili kuendelea kufanya utafiti kwa sababu tunachoamini kwamba bado yapo maeneo ya vivutio vya watalii inawezekana bado hatujayavumbua yakiwemo maeneo ya kihistoria ya hiyo historia utumwa na vitu vingine. Sasa kuendelea kuyatangaza, kwa sababu kuwa nayo na kuyavumbua ni suala moja lakini kuendelea kuyatangaza ili walio nje na ndani ya nchi yetu waweze kutambua wapi wanaweza wakajifunza na wakapata kujua hiyo historia.

Mheshimiwa Spika, swali lingine, ni nini sasa matarajio yetu, Matarajio yetu ni kuhakikisha kwamba tunaongeza idadi kubwa ya watalii kutoka idadi tuliyo nayo kuendelea idadi kufika hata watalii milioni tano. Lengo na madhumuni ni kuongeza sasa mapato ya nchi.

Mheshimiwa Spika, ili tuweze kufikia hayo matarajio kwanza tuhakikishe kwamba tunatoa elimu kwa wananchi ili waweze kutambua umuhimu wa utalii wa ndani, lakini cha pili kutoa huduma bora hicho tumekipanga ili lengo na madhumuni wanapo kuja kujifunza waweze kupata huduma bora.

Mheshimiwa Spika,nakushukuru.
MHE. PROF. PATRICK ALOIS NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika,
Nakushukuru kwa kunipa tena fursa ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Je Serikali ina mpango gani wa kushirikisha jamii ya vijiji vyote vinavyozunguka mlima Kilimanjaro ili kutunza rasilimali ambazo zipo katika mlima huo?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, Maporomoko ya Materu au Materu water falls iliyopo katika mto Kware katika viunga vya Mlima Kilimanjaro ni kivutio kikubwa cha watalii;

Je, Serikali ina mpango gani kusaidia juhudi za wananchi katika kuboresha maporomoko hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa
Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Patrick Alois Ndakidemi Mbunge wa Moshi Vijijini kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, namna gani tunaweza tukawashirikisha wananchi; Ushirikisho wa kwanza ni kuendelea kuwapa elimu, kwa sababu tunaamini kwamba moja ya miongoni mwa mambo ambayo yanaweza yakahifadhi hili eneo au yakatoa huo ushirikiano wa kuwashirikisha wananchi au wanakijiji ni kuendelea kuwapa taaluma.

Mheshimiwa Spika, lakini cha pili ni kuanzisha na kuendeleza vikundi shirikikishi. Vikundi ambavyo vitasaidia katika kulinda haya maeneo. Lakini kingine, tumeona moja miongoni mwa njia ya kuweza kunusuru maeneo haya ni kuhakikisha kwamba tunawasisitiza wananchi wanaendelea kupanda miti kwa wingi. Kikubwa zaidi tunaendelea kuwaomba wananchi wa maeneo yale waache kufanya shughuli za kibinadamu katika maeneo yale ya Mlima Kilimanjaro, zikiweno shughuli za Kilimo, shughuli za ukataji miti lakini mwisho wa siku wanakwenda kuchoma miti pale na hatimaye inapelekea majanga makubwa. Kwa hiyo hiyo ni sehemu kubwa ambayo tumeichukua kama hatua ya kuwashirikisha wanakijiji.

Mheshimiwa Spika, lakini swali la pili katika suala la kuboresha na kutunza hichi chanzo cha maji cha Materu Water Falls, cha kwanza tunaendelea kutoa elimu kama kawaida yetu kwa sababu tuna amini elimu ndiyo itakayokitunza kile chanzo. Cha pili tumesisitiza watu waendelee kuipanda miti pale kwa sababu kisayansi miti ile ndiyo inayokwenda kuvuta mvua ile na tayari kile chanzo kina imarika. Kikubwa tunaendelea kusisitiza Wananchi wasifanye shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya vyanzo vya maji mwisho wa siku wanaharibu hivyo vyanzo.
MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niishukuru Serikali kwa jibu lake lakini pia wamekuwa wanasiasa. Mimi ombi langu ni hili; kwa sababu hili siyo jambo la kupanga ni jambo la dharura, na tumeliuliza zaidi ya miaka mitatu humuhumu ndani majibu ndiyo hayahaya, ombi langu ituambie Serikali.

a) Je, ni lini imeamua au itaamua kulishughulikia jambo hili kwa dharura?

b) Je, ni lini sasa Serikali itashirikiana seriously na Serikali ya Zanzibar ili kuwaondolea maafa watu wetu wa Mwera?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Zahor Mohammed Haji, Mbunge wa Jimbo la Mwera kutoka Zanzibar kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, tayari ziko hatua mbalimbali ambazo zimeshachukuliwa kama hatua za dharura kwa sababu ya jambo hili la utokeaji wa haya maafa. Na hapa nataka nichukue fursa hii nimpe pole sana Mheshimiwa Zahor kwa haya matukio ambayo yanatokezea mara kwa mara.

Mheshimiwa Naibu Spika, kitendo cha Serikali kuunda kamati zinashughulikia maafa ambazo zipo kwenye ngazi tofauti, zikiwemo ngazi za shehiya na ngazi za wilaya ni miongoni mwa hatua madhubuti ambayo imeshachukuliwa. Katika jibu la msingi tayari tumeshaeleza kwamba, kupitia bajeti hii ya mwaka ya fedha huu 2023/2024 tutahakikisha kwamba tunakwenda kushughulikia maeneo yote ambayo yanakabiliwa na maafa kama haya likiwemo Jimbo la Mwera na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nataka tu nimwambie Mheshimiwa kwamba kuna baadhi ya mambo tayari tumeshayaelekeza. Serikali imetoa maelekezo kupitia Serikali ya Jamhuri na Serikali ya Zanzibar, kwamba kwanza watu waendelee kupewa elimu, ngazi za shehiya, halmashauri, wilaya, mikoa zitoe elimu kwa wananchi. Elimu ya kwanza, wananchi wasijenge kwenye mabonde, wasijenge kwenye maeneo ambayo maji yanatuama. La pili, wananchi wasitupe taka chafuzi, taka ngumu, taka zidishi kwenye maeneo ya mitaro, mwisho wa siku inakwama, halafu maji hayaendi yanasababisha mafuriko. La tatu, wajenge kwenye maeneo ambayo yameshapimwa. Lengo na madhumuni wajenge kwenye maeneo salama waepukane na maafa kama haya, nakushukuru.
MHE. FATUMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuweza kuuliza swali la nyongeza. Eneo la Nkuhungu katika Jiji la Dodoma ni miongoni mwa maeneo ambayo yanaathiriwa sana na mafuriko mara kwa mara. Nini mkakati wa Serikali wa kutengeneza miundombinu mizuri ili kuwanusuru na mafuriko wananchi hawa wa eneo la Nkuhungu? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mama Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yapo maeneo ambayo hali iliyofikia sasa hakuna namna nyingine isipokuwa ni kutengenezewa miundombinu ambayo itakwenda kudhibiti hii hali na kuwaacha wananchi wakiwa salama. Nimwambie Mheshimiwa kwanza tutataka tufanye study, tufanye utaratibu maalum wa kufanya tafiti kujua nini kinatakiwa hapo, kama ni daraja au ni kivuko kingine chochote.

Mheshimiwa Naibu Spika, cha pili, tutafute fedha sasa, kwa sababu hivi vitu vinataka fedha. Nimwambie Mbunge awe na Subira, maeneo yote ambayo yanaelekea ama yameshaingiliwa na maji na yanasababisha mafuriko hasa kipindi cha mvua kubwa, Serikali kwa kupitia ofisi yetu itahakikisha kwamba tunayashughulikia, nakushukuru. (Makofi)
MHE. HALIMA J. MDEE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Jimbo la Kawe katika maeneo ya Boko Basihaya, Boko Magengeni, Mto Nyakasangwe ni maeneo ambayo yamekuwa yakikumbwa na mafuriko kwa muda mrefu sana. Awamu ya Mheshimiwa Jakaya walishakwenda pale, Awamu ya Mheshimiwa Magufuli wameshakwenda pale na sasa hivi ni Awamu ya Sita. Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na kero hii kubwa inayosumbua wananchi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Halima Mdee, Mbunge wa Kawe, kama ifuatavyo: - (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kwamba azma ya Serikali hii ya Mama Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kwamba inatekeleza ahadi ambazo zilishaahidiwa, inatekeleza kwa vitendo Ilani ya Uchaguzi. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutafanya kadri itakavyowezekana kuhakikisha kwamba tunakwenda kutengeneza miundombinu rafiki, itakayoondosha hiyo changamoto ya mafuriko na changamoto nyingine ambayo inakuwa ni kikwazo katika maendeleo ya kiuchumi hasa ya wananchi,, nakushukuru.
MHE. NORAH W. MZERU: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Nashukuru kwa majibu mazuri ya Serikali. Nina maswali mawili ya nyongeza.

Je, ni lini Serikali itawekeza fedha kwenye kuutangaza Mlima Uluguru kama kivutio kizuri cha utalii?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Kwa kuwa maporomoko haya yanaleta mvutio mkubwa kwa utalii.

Je, ni lini Serikali ina mpango wa kuyatunza na kuhifandhi mazingira yaliyozunguka maporomoko hayo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kama tutapita vizuri kwenye Jibu la msingi tulisema kwamba Serikali kupitia mfuko wa UVIKO tayari tulishawekeza pale takribani shilingi 214.3 ilikuwa lengo na madhumuni ni kujenga ile miundombinu ya barabara ya kilomita nane kutoka barabara kuu kuelekea kwenye kivutio hichi. Lakini kiubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti yetu ambayo tunategemea kusoma hivi karibuni tutahakikisha kwamba tutatenga fungu maalumu la kutengeneza miundombinu rafiki katika kituo ama katika kivutio hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini suala la pili nimwambie tu kwamba ipo mikakati kabambe ambayo Serikali na Wizara tumeshaichukua kuhakikisha kwamba tunatunza mazingira katika eneo hili. Tumeshakaa sisi ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii, lakini pia tumeshakaa na watu wa Halmashauri pamoja na TFS kuhakikisha kwamba, la kwanza tunakwenda kupanda miti ya kutosha, lakini tulishatoa maelekezo kwa kuwaambia wananchi waliozunguka maeneo yale kwamba wasifanye shughuli zozote za kibinadamu katika meneo yale, ikiwemo za ufugaji, kilimo na nyingine. Lengo na madhumuni ni ili tutunze kivutio, tuvute watalii lakini pia tuongeze pato, nakushukuru.
MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Naibu Waziri kwa majibu yake mazuri ya kutia moyo lakini pia nimpongeze Rais, Samia na Rais Mwinyi, kwa kutatua kero za Muungano hadi hadi kufikia 22 na kubakia kero nne. Swali langu ni kwamba kuna kauli gani ya Serikali juu ya kutatua hizo kero nne zilizo baki?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali langu la pili; Serikali imejipanga vipi kwa ajili ya utoaji elimu juu ya suala la Muungano kwa vizazi vijavyo? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kwanza zinaendeleza ushirikiano ama zitaendeleza ushirikiano wa kuhakikisha kwamba changamoto zote zinazogusa kwenye Muungano zinatatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukasema kwamba ili kuhakikisha kwamba tunatatua changamoto hizi, ziko Kamati ambazo zimeundwa au iko Kamati ya majadiliano ya pamoja ambayo ndio inayosimamia utatuzi wa changamoto hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba pamoja na kwamba zipo changamoto zilizobakia lakini kwa kushirikiana na kamati hii tunakwenda kumaliza changamoto zote ili Muungano wetu huu saa uwe imara na uweze kudumu kwa muda mrefu. Kwa maana kwamba kuna Kamati za wataalam, Kamati za Makatibu Wakuu, Kamati za Mawaziri lakini kuna Kamati za Viongozi wakuu ambao hukaa kwa ajili ya kutatua changamoto hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba baada ya kuwa tumetatua changamoto hizi, kinchofuata sasa ni kuwajulisha na kuwaeleza wananchi hatua tuliyofikia kama Serikali. Tumeanza na vyombo vya habari kuwaelimisha wananchi juu ya changamoto zilizokuwepo na zilizobakia. Kingine tumetoa tovuti maalumu www.vpo.go.tz wananchi wakienda hapo wanaweza kuona changamoto zilizotatuliwa na zile ambazo bado hazijatatuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumefanya makongamano mbalimbali ambayo tumekuwa tukitoa elimu kuhusiana na masuala Muungano, nakushukuru.
MHE. ASYA MWADINI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Kwa maelezo ya Waziri kwamba hakuna changamoto mpya ni kumshukuru Mwenyezi Mungu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto za zamani bado hazijakamilika. Ikiwemo hasa changamoto ya bandari na hili suala la bandari limekuwa linaleta kelele nyingi kwa wananchi na limekuwa kero kubwa. Kwa nini Serikali haioni haja ya kulichukulia jambo hili kwa udharura wake na kulitatua haraka iwezekanavyo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge. Katika kikao chetu ambacho tulikaa mwezi wa sita tulikubaliana na tulitoa maelekezo. Kwa sababu vikao hivi huwa tunakaa na Wizara za pande zote mbili au pande zote mbili zinagusa Muungano. Tulitoa maelekezo na maelekezo haya yamekwisha anza kufanyiwa kazi kwamba, watu wa TRA na wengine wa Bandari wanaohusika waende wakakae washughulikia hili jambo, tuweze kuambizana zipi zitakuwa zinalipiwa kama sehemu ya changamoto na zipi hazilipiwi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa kwa kuwa Kamati zinaendelea kukaa, hili jambo tunakwenda kuzimaliza ili kuimarisha Muungano wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. KHALIFA MOHAMMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa changamoto ambazo bado hazijatatuliwa ni upelekaji wa sukari ya Zanzibar katika soko la Tanzania Bara. Ni lini kero hii ambayo ni ya muda mrefu itatatuliwa?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba moja ya miongoni mwa mambo ambayo Kamati zimo mbioni kuhakikisha kwamba tunaliweka sawa ili kuondosha hii kama ni sehemu ya changamoto ya Muungano ni hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo hili ni jambo ambalo kama tulivyosema hapo awali kwamba jambo hili la utatuzi wa changamoto za Muungano limetengenezewa kamati maalumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe waheshimiwa Wabunge, ikiwa tumeweza kutoka tangu changamoto ya kwanza leo tumezipata changamoto 22 maana yake na hili kupitia Kamati zinazohusika kwa mujibu wa taratibu zote linakwenda kutatuliwa ili kupunguza changamoto kubwa ambayo inakabili Muungano wetu.
MHE. ZAHOR MOHAMMED HAJI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishukuru Serikali kwa jibu. Pamoja na kwamba jibu hili limejibiwa kisiasa zaidi kuliko tatizo lilivyo, ningeomba Mheshimiwa Waziri atuambie ni lini sasa Serikali au Wizara itakuwa Serious Kujibu matatizo yetu ambayo yanaongozwa na Sheria? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili; kwa sababu imeonekana Sheria hii inafanya kazi zaidi kwenye upande mmoja lakini kuwaathiri Wabunge wa Majimbo kwa upande wa Zanzibar. Je, Serikali sasa haioni iko haja ya kuwaandikia wenzetu wa Zanzibar ili waache kuvunja Sheria iliyotungwa na Bunge hili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, najibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira tuko serious katika kufanya kazi zetu. Tupo serious kufanya kazi zetu kwa mujibu wa sheria na taratibu zote zilizowekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii inayafnya kazi kwa upande huu wa Mfuko wa Jimbo iko Sheria inayosimamia Mfuko wa Jimbo. Lakini ipo Sheria inaitwa Zanzibar Revenue Administrative Act. Sheria ambayo inasimamia na imetoa mamlaka kwa halmashauri na Mabaraza ya Miji kutoza ama kukata kodi kutokana na sehemu ya fedha zinazoingia kwenye halmashauri zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko serious na kutokana na u-serious tulionao tunakwenda kutatua changamoto zote ambazo zinakabili Mfuko wa Jimbo hasa katika Jimbo la Mwera na maeneo mengine yote kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini swali la pili, nimwambie Mheshimiwa kwamba tuko tayari kama ushauri wake alivyosema kwamba tuandike barua lakini nataka nimfahamishe tunavyo vikao vinavyohusika na kujadili changamoto hizi na majadiliano yote yanayohusiana na Mfuko wa Jimbo. Vikao ambavyo vinaanza katika ngazi nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tayari tumekwishaandaa kikao kazi ambacho tunakwenda kukaa viongozi wa halmashauri zote, viongozi wa mabaraza ya miji, Ofisi ya Makamu wa pili wa Rais ili lengo na madhumuni na Wabunge wote tuweze kuelezana hizi changamoto zinazogusa Mfuko wa Jimbo hasa kwa upande wa Zanzibar.
MHE. AMINA DAUDI HASSAN: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Swali la kwanza; licha ya majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi katika fukwe za hindi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikishirikiana na Serikali ya Zanzibar, je, haioni haja ya kujenga kuta kandokando ya bahari ili kuzuia uendelezaji wa athari za mabadiliko ya tabianchi? Mfano kama Nungwi, Jambiani, Paje na vijiji vingine vyote vyenye fukwe ya bahari? Ahsante .
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya Mheshimiwa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa na mpango kabambe na mipango mingi ya kuhakikisha kwamba, tunakabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi, hasa katika maeneo ya fukwe, ama maeneo haya ya ukanda wa Bahari, hasa katika Bahari ya Hindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza, tumekuwa tunahamasisha jamii ambazo zinaishi humu pembezoni mwa bahari, hasa maeneo ya ufukwe, kwanza kurejesha ama kupanda mikoko ambayo ilikuwepo lakini imekatwa, lakini hatua nyingine ambayo tumeichukua kama sehemu ya mpango kabambe wa Serikali ni kuendelea kuwaambia wananchi kwamba, wasiendelee kutupa taka hatarishi, lakini vilevile kufanya shughuli za uchimbaji wa mchanga katika maeneo haya ya fukwe. Kikubwa zaidi tumekuwa tuykiwaeleza shughuli za uvuvi, lakini pia shughuli za ulimaji ama uvunaji wa mwani zisiharibu fukwe zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa suala la ujenzi wa kingo ama kuta za kuzuia maji ya bahari au maji ya chumvi yasiingie maeneo mengine, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tayari imeshaanza ujenzi wa ukuta kwa upande wa Tanzania Bara katika Mkoa wa Mtwara katika maeneo ya Mikindani, lakini kwa upande wa Kusini Pemba katika eneo linaitwa Sepwese, tayari tumeshaanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa maeneo ya Paje, Jambiani, Bwejuu, Nungwi na maeneo mengine, cha kwanza tunaenda kufanya utafiti kujua ni aina gani ya ukuta ambao unatakiwa, lakini tumwambie Mheshimiwa tunakwenda kutafuta fedha, ili tuone namna ambavyo tunakwenda kujenga hizi kuta ambazo zita-control uingiaji wa maji na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. FATMA TOUFIQ: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali la nyongeza. Waathirika wakuu wa suala zima la tabianchi ni wanawake na hasa wale wanawake wanaoishi maeneo ya pembezoni. Nini mkakati wa Serikali wa kuwa na program maalum kwa ajili ya hawa wanawake wa pembezoni waweze kupata mafunzo kukabiliana na hali ya tabianchi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Toufiq, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, tayari alichokiomba Mheshimiwa Toufiq tumeshakianza. Tumeanza na Mkoa wa Kaskazini Unguja, tayari kule viko vikundi vya akinamama vya ujasiriamali katika Jimbo la Chaani. Tumeshaanza hiyo program ya kuwapa taaluma akinamama ili waweze kujua namna bora ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Haya tumeyafanya kwa sababu, tumeona baadhi ya shughuli za uvuvi, lakini hata shughuli za ulimaji na uvunaji wa mwani, wengi wao tumegundua ni akinamama. Kwa hiyo, tumeona tuendelee kuwapa hii elimu ili waweze kuepukana na hizi athari za mabadiliko ya tabia nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. PROF. KITILA. A. MKUMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa jibu hilo kwa umakini huo ambao ameonyesha Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye jibu lake.

Je, lini atakuja kwenye Mtaa wa Kibangu Kata ya Makuburi ili kushughulikia changamoto ya uchafuzi wa mazingira kutoka kwenye Viwanda vya EPZA?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, najibu swali kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nipo tayari kwenda kuona uharibufu ambao umefanyika huko na badala ya hapo kukaa na wamiliki wa viwanda hao na kuwaeleza namna bora ya uhifadhi na utunzaji wa mazingira na uhifadhi wa wananchi, nakushukuru.
MHE. SIMAI HASSAN SADIKI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana, pamoja na majibu mazuri ya Serikali nina maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa sasa ni mwaka wa tatu nimekuwa nikisimama katika Bunge hili kuulizia jitihada zinazochukuliwa na Serikali zote mbili katika kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi maeneo ya Nungwi lakini majibu tunayopata leo ndiyo kwanza shilingi milioni 650 zimetengwa kwa ajili ya kufanya utafiti. Ninachotaka kujua ni lini utafiti huu utaanza?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili, shughuli za utalii na uchumi wa bluu zimekuwa zikiathiri sana ukataji wa mikoko katika maeneo ya fukwe za Bahari ya Hindi kule Zanzibar. Je, Serikali ina mpango gani wa dharura wa kuhakikisha kwamba mikoko inarejeshwa katika uhalisia wake? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza naomba kuchukua fursa hii kumpongeza sana kwa kuwa jambo hili amekuwa akilipigia kelele sana na hatimaye sisi kama Serikali tumeshaandaa fedha kwa ajili ya kuanza angalau tathmini ya awali.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa fedha hizi zimeshapatikana naomba kumwambia tu Mheshimiwa Mbunge kwamba sasa utafiti unaenda kuanza muda wowote. Kama tulivyosema kwamba kuna kuta za aina nyingi, kwa hiyo ni lazima utafiti ufanyike ili tujue ni aina gani ya kuta. Kuna kuta za slope ambazo zinatoa maji mitaani zinapeleka baharini, lakini pia kuna kuta ambazo zinakinga kutoka baharini maji yasije mitaani. Kwa hiyo ni vyema utafiti ufanyike ili tuone ni aina ya kuta na pia tuweze kupima current ya maji ya sea breeze na land breeze, ni aina gani ya huduma ambayo wananchi wanatakiwa wapatiwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama hilo halitoshi, kwa upande wa swali la pili, tumechukua hatua nyingi. Moja ni kuendelea kutoa elimu wasikate, wapande na wasichome mikoko ambayo ipo around ufukwe wa bahari. Kubwa zaidi tumeendelea kuhimiza kupitia ilani ambayo inasema kwamba kila Halmashauri kila mwaka lazima ipande miti milioni 1.5. Kupitia miti hii tumehimiza mikoko ipewe kipaumbele ili kunusuru fukwe zetu lakini zaidi kuendelea na ile sera yetu ya soma na mti. Tunataka wanafunzi wa sekondari, msingi, vyuo na vyuo vikuu wapande miti, lakini miti ambayo tumeipa kipaumbele hasa kwa shule za fukwe ni mikoko, nakushukuru.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kuniona. Kwa vile Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Muungano na Mazingira ndiyo ambayo inashughulika na masuala ya kuratibu na kushughulika na mabadiliko ya tabianchi. Nilitaka kujua je, mnatumia utaratibu gani wa kupokea miradi yote ambayo inatoka Zanzibar kwa ajili ya utekelezaji wa kushughulika na haya mabadiliko ya tabianchi kwa upande wa Zanzibar?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu ni kwamba kwanza tunaandaa maandiko ambayo yanalenga kwenye mradi husika. Kinachofuata sasa ni kufanya tathmini na utafiti wa kujua mradi ulioombwa na baadaye mradi huo unaanza utekelezwaji kama miradi iliyotekelezwa huko Zanzibar.
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru. Hivi karibuni Serikali imetangaza uwepo wa Mvua za El nino. Ni upi mkakati wa haraka wa Serikali kupunguza athari zitakazotokana na mvua hizi ndani ya Jiji la Dar es Salaam na hasa mafuriko ambayo yanasababishwa na Mto Msimbazi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kipindi cha mvua kubwa mara nyingi kunakuwa na mafuriko makubwa ambayo yanasababisha athari hasa kwenye makazi ya wananchi. Wakati mwingine inafika hatua mafuriko yanagharimu maisha ya wananchi. Namwambia Mheshimiwa kwamba huwa tunachukua hatua nyingi. Moja, ni kuelimisha wananchi; kwa mfano sasa hivi tumeanza kutoa elimu kuhusu Mvua za El nino ambazo zinategemea kuja. Tunawaambia wananchi wasijenge kwenye maeneo au karibu na maeneo ambayo yanajaa maji ili kama wana mpango huo waanze kuondoka mapema ili zitakapokuja mvua wasiweze kupata mafuriko hayo ama mafuriko hayo kuleta athari kwa wananchi. (Makofi)
MHE. BONNAH L. KAMOLI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka kumuuliza Mheshimiwa Naibu Waziri, ni lini Serikali itaanza kujenga Mto Msimbazi ukizingatia sasa hivi wataalam wa hali ya hewa wamesema kwamba kuna mvua kubwa inanyesha; je, ni lini wataanza kutujengea ili wananchi wetu wawe salama? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba ujenzi wa Mto Msimbazi umeanza, na nimwambie tu Mheshimiwa kwa kuwa ujenzi huu...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Waziri umeanza au uko katika maandalizi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hatua tuliyofikia maana yake sasa tunakwenda kuanza.

NAIBU SPIKA: Haya, endelea.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo namwambia Mheshimiwa kwamba uanzaji huu unakwenda kwa hatua. Hatua hizi zinakwenda kadri tutakavyokuwa tunapata fedha. Tutahakikisha kwamba maeneo yote yatajengwa na tutahakikisha kwamba tunapata usalama wa wananchi.
MHE. MWANTAKAJE HAJI JUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa majibu mazuri ya Serikali. Nilikuwa na swali moja, hiki kituo ni chakavu na cha miaka mingi, miundombinu yake ni mibovu; je, Naibu Waziri yuko tayari kuongozana nami kwenda kujionea kituo hicho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Serikali ama Wizara ya Mambo ya Ndani tupo tayari kuja kukagua na kuona uchakavu wa kituo hicho ili kuona namna ya kuweza kupata hizi fedha na kuanza kukifanyia ukarabati, nakushukuru.
MHE. ZUENA A. BUSHIRI: Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na majibu mazuri ya Serikali, ninayo maswali mawili ya nyongeza.

Je, Serikali ina mpango gani wa muda mfupi wa kuwakosoa au kuwasaidia wananchi hawa ambao ni Maaskari wetu wanaofanya kazi usiku na mchana ambao wanaishi katika mazingira magumu sana, kwa kuwa nyumba zao zinavuja na miundombinu imechoka sana?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu la pili. Je, Mheshimiwa Naibu Waziri yuko tayari kuongozana nami kwenda eneo la tukio akaone hali halisi ya makazi ya maaskari wetu wanavyoishi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu maswali ya nyongeza ya Mheshimiwa Zuena Athumani kuwa Serikali inatambua uchakavu wa Vituo vya Polisi lakini pia inatambua uchakavu wa nyumba za makazi kwa ajili ya askari hawa. Aidha, Serikali inatambua juhudi na kazi kubwa inayofanywa na Jeshi la Polisi katika ulinzi na usalama wa raia na mali zao.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie Mheshimiwa Mbunge, kwa sasa tunaenda kuzitafuta shilingi bilioni 3.6, zitakapopatikana tunaenda kuanza ujenzi wa nyumba hizo, lengo na madhumuni ni Askari wetu waweze kuishi kwenye mazingira mazuri. Aidha, nimwambie tu kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, tupo tayari kuambatana naye kwenda mpaka kwenye eneo ili kukagua na kuona uchakavu huo na kuona namna ya kuweza kuwasaidia, nakushukuru. (Makofi)
MHE. ROSE V. BUSIGA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nami naomba niulize swali la nyongeza. Katika Mkoa wetu wa Geita kuna nyumba nyingi sana za Askari ambazo ni chakavu; je, Serikali ina mpango gani wa kuweza kukarabati nyumba hizo za askari ili askari wetu wa Mkoa wa Geita waweze kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rose, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesema hapo awali kwamba kwa sasa Serikali tunatafuta fedha na zitakapopatikana, pamoja na maeneo mengine yenye uchakavu wa nyumba na vituo, tutahakikisha kwamba Mkoa wa Geita nao tunautazama, lengo na madhumuni sasa wananchi waweze kupatiwa huduma hizo vizuri zaidi, nakushukuru.

MHE. JESCA J. MSAMBATAVANGU: Mheshimiwa Naibu Spika, hali ya makazi ya polisi katika Kituo Kikuu cha Iringa Mjini ni mbaya sana na majibu ya Naibu Waziri ni kwamba mpaka fedha zitafutwe. Nilitaka kujua wale askari wataendelea kuishi wapi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, jukumu la ulinzi na usalama katika Tanzania yetu ni jukumu la kila mtu na jukumu la kusaidia kuona kwamba huduma zinapatikana ni jukumu la Serikali lakini pia ni jukumu la viongozi. Namwomba basi angalau Mheshimiwa Mbunge naye aanze kuonesha mfano halafu sisi kama Serikali tutakuja kuongezea ili tuone namna ambavyo wananchi wanaweza kupata huduma hizo, nakushukuru. (Makofi)

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya swali la nyongeza. Mheshimiwa Waziri katika Kituo cha Polisi Wilaya ya Rungwe Tukuyu Mjini, hawana ukuta wa kutenganisha kituo cha polisi na shule ya msingi ili kuzuia watoto wadogo kuona jinsi wahalifu wanavyopelekwa kwenye kituo.

Je, ni lini Serikali mtawajengea ukuta wa kuzunguka ili waweze kuwa katika sehemu yao binafsi pekee kama polisi? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba mara nyingi vituo hivi tunatakiwa tuviweke katika mazingira ambayo yanaweza pengine ingawaje vinatoa huduma kwa jamii, lakini jamii isiweze kuweza kuona mambo yanayoendelea pale lakini zaidi kuweza kukitengenezea mazingira ya usalama zaidi kile kituo. Nimwambie tu Mheshimiwa Sophia kwamba tunafanya juhudi za kutafuta fedha. Tutakapopata fedha hizo, tutakwenda kujenga uzio huo ili tuweze kutenganisha hayo maeneo, nakushukuru. (Makofi)
MHE. MBAROUK JUMA KHATIBU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

(a) Je, hatuoni kuna haja ya kuharakisha ujenzi huu kutokana na uhalifu ambao unajitokeza?

(b) Je, Serikali haioni haja ya kuongeza nguvu ya askari na gari kwa ajili ya doria? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, najibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Khatibu, Mbunge wa Jimbo la Bumbwini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kumpongeza sana kwa kazi nzuri anayoifanya; lakini kikubwa nimwambie tu kwamba kuna haja ya kufanya haraka ya kituo hiki ipo na tayari Jeshi la Polisi kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi tumeshawasiliana na wenzetu wa Mamlaka ya Bandari – Zanzibar ili ikiwezekana haraka waweze kuanza ujenzi wa kituo hiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, niwaambie tu siyo kituo hiki, pale bandarini ni lazima pale pawe na watu wa uhamiaji, pawe na ofisi za fire na hicho kituo cha polisi ili lengo na madhumuni ni huduma za ulinzi na usalama katika eneo lile zipatikane.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine, haja ya kuongeza askari ipo. Nimwambie tu Mheshimiwa awe na subira kidogo kwa sababu, vijana wetu bado wapo kwenye mafunzo. Juzi tu Jeshi la Polisi walitangaza nafasi nyingine ili lengo na madhumuni tuongeze nguvu ya ulinzi na usalama katika maeneo yetu yote ya Tanzania, ninakushukuru.
MHE. DKT. CHRISTINA C. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali la nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa Kata ya Isalamagazi ambayo ndiyo Makao Makuu ya Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kuna kituo cha polisi ambacho kimejengwa enzi za mkoloni.

Je, ni lini Serilkali itajenga kituo hicho? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali inatambua uchakavu wa baadhi ya vituo vya polisi na hata baadhi ya makazi ya Askari Polisi. Ndiyo maana Serikali tumo kwenye mbio ya kuhakikisha tunatafuta fedha ili tujenge vituo vya kisasa zaidi na viweze kutoa huduma kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu Mheshimiwa kwamba Serikali tutakapopata fedha tutahakikisha kituo chake tunakipa kipaumbele ili wananchi waweze kupata huduma za ulinzi na usalama. Ninakushukuru.
MHE. GRACE V. TENDEGA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Ninaomba sasa niulize maswali mawili ya nyongeza.

a) Je, ni kwa nini Serikali inachukua muda mrefu kutoa vitambulisho kwa Watanzania, hamuoni kwamba mnawakosesha fursa mbalimbali ambapo kitambulisho ndiyo takwa la fursa hizo?

b) Je, ni lini Serikali itaoanisha data zote za msingi ili ziweze kusomeka kwenye kitambulisho hicho cha NIDA?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, ninashukuru sana kwa maswali haya mawili ya nyongeza. Naomba kutoa majibu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Matiko, amekuwa mara kadhaa akifuatilia kuona namna ambavyo Watanzania wanaweza kupata vitambulisho ili kuweza kupata huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali haijachukua muda mrefu sana kutoa vitambulisho kwa watu; na kama imechukua basi tulikuwa tuna changamoto. Changamoto ya kwanza tulikuwa na upungufu wa mashine za kisasa ambazo zilikuwa zinatoa vitambulisho kwa speed kubwa. Niwaambie wananchi na Watanzania; sasa tumeshapata mashine bora za kisasa na tunakwenda kuhakikisha Watanzania wote wanapata vitambulisho ili waweze kupata huduma, kwa sababu tunatambua sasa hivi kila kitu ni kitambulisho.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto nyingine. ninawomba Watanzania wote, wakamilishe taratibu ili tuweze kupata vitambulisho. Kuna watu wanashindwa kutoa baadhi ya particulars muhimu za kutengenezewa vitambulisho. Inakuwa ngumu kwetu kuweza kuwakamilishia.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeona kwamba tunavyo vitambulisho vingi. Tuone namna ya kuviunganisha vitambulisho hivyo ili kiwe kimoja. Maana yake hicho hicho kiwe na uwezo wa kutumika benki, kwenye passport unaweza ukawa unakitumia kama NIDA au kitambulisho kingine. Tuko mbioni kuona namna ambavyo Serikali itapunguza changamoto hiyo, ninakushukuru.
MHE. ABUBAKARI D. ASENGA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Naipongeza Serikali kwa nia yake ya kuwa tayari kwa mafunzo haya, na Wabunge wengi tulioenda katika yale mafunzo tulikuwa tunapata maswali mengi sana ya Wakuu wa Idara na baadhi ya Wakuu wa Wilaya na Wakurugenzi wanaotaka kwenda kwa kujitolea, walikuwa wanauliza ni utaratibu gani ambao wanaweza kuufuata ili kushiriki mafunzo haya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru sana Kambi ya Makutupora hapa, imetupa mafunzo mazuri sana na tunatoa ombi kwa Wabunge ambao hawajaenda waende kwa sababu kila siku wanatuambia kwenye group kwamba vifaa vyao viko pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, maswali yangu mawili ya nyongeza. La kwanza: Je, ni lini intake nyingine ya Wabunge na viongozi wa wilaya ambao wako tayari itaenda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili. Kama nilivyosema, Kambi ya Makutupora iko hapa Dodoma, ni kaibu: Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza fedha ya bajeti kwa sababu JKT ni taasisi ya Kiserikali ili Kambi ile jirani ya Makutupora iweze kutoa mafunzo vizuri zaidi na kwa ufanisi zaidi, ikiwemo kujenga mabweni, vitanda na kadhalika?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Abubakari Damian Asenga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba Waheshimiwa Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania mara kadhaa wamekuwa wakienda kwenye kambi hizi kwa ajili ya kushiriki kwenye mafunzo haya ambayo yana nia ya kuwajenga Waheshimiwa Wabunge. Ni kweli kwamba wapo baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hawajapata fursa hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa niwaambie tu kwamba mara nyingi sababu zinazosababisha hizi, kwanza ni nafasi yetu sisi kama Waheshimiwa Wabunge kwa sababu ya majukumu ambayo tunayo. Lingine kubwa ni kutokana na utaratibu. Nawaomba Waheshimiwa Wabunge kupitia Bunge hili, kama tulivyoeleza katika jibu la msingi, iombwe ruhusa, kwa maana ya kwamba tuombwe kibali maalum ili Jeshi la Kujenga Taifa liweze kutoa fursa hiyo ya Wabunge wengine kuweza kuendelea ama kupata mafunzo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine niseme tu kwamba, kwa kuwa mafunzo haya yamelenga katika kuwajengea uzalendo, kuwajengea utayari, ukakamavu na ujasiri Waheshimiwa Wabunge na viongozi wengine wa taasisi nyingine, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajitahidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyoelezwa katika jibu langu la msingi, kwamba suala la uchangiaji gharama ni jambo la msingi; na kwa sababu tunatakiwa tuchangie gharama hizi kwa sababu ya mahitaji maalum yakiwemo afya, matibabu, chakula na vifaa vingine, lakini nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba katika bajeti inayofuata tutajitahidi tuongeze fungu maalum kwa ajili ya kutoa huduma hizi za mafunzo kwa Waheshimiwa wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.
MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipata nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali namba moja, kwa kuwa NEMC ndiyo taasisi pekee Tanzania ambayo ina uwezo wa kuomba fedha kupitia huu mfuko wa kuhimili athari za mabadiliko ya tabianchi. Je, Serikali inashirikishaje taasisi nyingine pamoja na NGO katika kuwajengea uwezo ili waweze kuomba fedha na kuzipata kwa haraka?

Swali namba mbili; Je, kwa kuwa Zanzibar fedha hizi pia zinatumika. Je, Serikali haioni haja ya kusaini memorandum of understanding na taasisi moja Zanzibar kama vile ZEMA ili kuweza kuimarisha uratibu na kuwajengea uwezo Wazanzibar ili fedha hizo ziweze kutumika kwa ufanisi zaidi? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano Mazingira hasa kupitia Baraza la NEMC tunao utaratibu wa kutoa uelewa kwa wale ambao wanakuja kuandika miradi na kuileta kwetu, zaidi wale ambao watakuja na miradi endapo miradi hiyo itakuwa haijakamilika taarifa zake, hapo ndipo tunawaita na kuwapa uelewa na kuwafahamisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kama kutakuwa na taasisi inataka kuandika miradi na hasa inataka kuleta kwetu basi tupo tayari kwenda kuwapa uelewa ili lengo na madhumuni wawe na ujuzi na utaalam mzuri wa kuandika miradi ambayo itakwenda kusaidia kutatua changamoto za wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Zanzibar tunao ushirikiano na usimamizi mzuri sana wa fedha za miradi na ndiyo maana miradi mingi haijakwama na inaendelea vizuri kwa upande wa Zanzibar na upande wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutaendeleza ushirikiano huo ili lengo na madhumuni tutatue changamoto za wananchi hasa za kimazingira na zile ambazo zina lenga katika kubaliana na mabadiliko ya tabianchi. Nakushukuru.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi kuniona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mradi ambao unatekelezwa kwenye Halmashauri ya Wilaya ya Kaskazini ya Unguja kwa upande wa Zanzibar, mradi huo wa EBA ambao umedhaminiwa kupitia Mfuko huo ambao Mheshimiwa Waziri umetamka mradi wa EBA lakini mradi huo utekelezaji wake ilikuwa ni 2018 mpaka 2022, ukomo wa mradi huo tayari umeshakamilika.

Je, Wizara yako ina mpango gani sasa wa kuhakikisha kwamba mradi ule ambao tayari uko kule Wilaya ya Kaskazini Unguja kwenye Vijiji vya Matemwe na Shehia ya Mbuyutende unakamilika? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, najibu swali la Mheshimiwa Usonge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwaambie Watanzania kwamba azma ya Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan ni kuhakikisha kwamba inatatua changamoto zote zinazokabili wananchi hasa changamoto zinazokabili kwenye upande wa mabadiliko ya tabianchi. Azma nyingine kubwa ni kuhakikisha kwamba miradi yote iliyokwishaanzishwa kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, ikiwa inasimamiwa na fedha kutoka nje, tutahakikisha kwamba miradi hii inakamilika ili sasa iweze kunufaisha wananchi na wananchi waweze kunufaika na hiyo miradi na mambo mengine yaende. Nakushukuru.
MHE. COSATO D. CHUMI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi.

Mifuko hii ambayo inatenga fedha kwa ajili ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi iko mingi na Mheshimiwa Rais aliposhiriki mkutano kule Scotland aliwasisitiza Mataifa makubwa waheshimu ahadi zao na kutenga hizo fedha. Tatizo na changamoto imekuwepo katika kukosa utaalam.

Je, Wizara iko tayari kuvishirikisha Vyuo Vikuu, Chuo Kikuu cha Dodoma, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, SUA na Chuo Kikuu cha Zanzibar katika kupata ule utaalam wa kuandika hayo maandiko ili tupate hizo fedha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, takribani miradi mingi tumekuwa tunawashirikisha wataalam hasa wataalam kutoka Vyuo Vikuu. Tumekuwa na miradi mingi na miradi hii mara nyingi kwenye masuala ya utafiti tunawashirikisha wanafunzi na walimu wa vyuo vikuu, hata kwenye masuala ya maandiko ya hii miradi kwa maana ya hizo proposal pia huwa tunawapa nafasi ya kuchukua mawazo yao ili lengo na madhumuni tuweze kupata mawazo ya kitaalam kwenye miradi hii, kwa sababu wenzetu wanapokuja kukagua miradi hii huwa zaidi wanaangalia utaalam ambao tumeutumia na zile pocedure ambazo tumezipitia katika kuimarisha miradi hii. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tuko tayari na kwa sababu tumeshaanza hilo jambo. Nakushukuru.
MHE. DKT. FLORENCE G. SAMIZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Kwanza kabisa naishukuru Serikali kwa majibu mazuri ambayo yameonesha matumaini kwa kuwa wameshafanya tathmini, lakini, je, Serikali haioni kwamba iko sababu ya kuharakisha ukarabati wa nyumba hizi ili kuboresha ufanisi wa askari angalau kwa kuanza na pesa kidogo mwaka huu, then mwaka kesho tumalizie? Ahsante sana. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, haja ya kufanya haraka ya kuharakisha upatikanaji wa hizi huduma ni jambo la msingi na sisi kama Wizara tutahakikisha kwamba tunakwenda kutafuta fedha kokote ziliko ilimradi tuhakikishe kwamba Vituo vya Polisi nchini kote ikiwemo Jimbo la Mheshimiwa Mbunge la Muhambwe vituo hivi vifike.

Mheshimiwa Spika, hii ni kwa sababu ya azma njema ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha kwamba kwanza wananchi wote wanapata huduma za ulinzi na usalama, lakini pia kuhakikisha kwamba tunaboresha mazingira yawe mazuri zaidi kwa upande wa vyombo hasa Jeshi la Polisi ikiwemo magari na Vituo vya Polisi na nyumba za makazi, nakushukuru.
MHE. DOROTHY G. KILAVE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Je ni lini Serikali sasa itamaliza nyumba za askari eneo la Barracks Kilwa Road ndani ya Jimbo la Temeke?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nataka nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba azma ya Serikali ni kuhakikisha kwamba Vituo vyote vya Polisi ikiwa vya Wilaya ikiwa vya Mikoa itahakikisha kwamba vinakamilika, lengo na madhumuni wananchi wajue sasa wapi wanakwenda kupeleka changamoto zao, kwa sababu tumegundua bado kuna baaadhi ya maeneo yakiwemo wilaya na maeneo mengine bado hayajapata Vituo vya Polisi. Kwa hiyo nimwambie tu Mheshimiwa kwamba tutahakikisha kwamba Kituo cha Polisi kinakuja na fedha zitakapopatikana, tutahakikisha kwamba tunampa kipaumbele kwa ajili ya kupata hicho Kituo cha Polisi.

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Je, ni lini Serikali itajenga Kituo cha Polisi katika Wilaya ya Uvinza?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, inatambua umuhimu wa uwepo wa Kituo cha Polisi katika Wilaya ya Uvinza. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajitahidi. Kokote tutazitafuta fedha zilipo ili tuhakikishe kwamba tunapeleka Kituo cha Polisi katika Jimbo lake ili mradi wananchi waweze kupata huduma za ulinzi na usalama na mambo mengine ya kipolisi, nakushukuru.

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi. Je ni lini Serikali itaweka bayana mpango mzima wa ukarabati au ujenzi wa Vituo vya Polisi pamoja na nyumba za kuishi kwa nchi nzima ili kuepuka kudaiwa huduma hii kila kukicha?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, nataka nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tayari tumeshaanza kufanya tathmini ya kuona namna ambavyo tunaweza tukauandaa huo mpango. Kwa hiyo nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajitahidi kadiri iwezekanavyo tuone namna ambavyo tunauhangaikia huo na kuweza kuanza kuufanyia kazi kama ambavyo Mheshimiwa ametaka. (Makofi)
MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Katika Kijiji cha Mkundoo na Mkusinde kumekuwepo na matukio kadhaa yameripotiwa ya uhalifu. Je, Serikali ina mpango gani wa kujenga Kituo cha Polisi eneo hilo?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tumekuwa tukiripotiwa baadhi ya matukio ambayo mengi yao yamekuwa yakisababishwa na wananchi wenyewe kwa wenyewe, lakini nimwambie tu kwamba Serikali haijalala kwa maana kwamba ipo makini kuhakikisha kwamba tunapambana dhidi ya vitendo vyote vya uhalifu ikiwemo na kuhakikisha kwamba tunatafuta magari kwa ajili ya kufanya doria na ukaguzi wa mara kwa mara ikiwemo na kujenga Vituo vya Polisi kwa ajili ya wananchi ili kuweza kwenda kupeleka changamoto zao na kuweza kutatuliwa kwa haraka, nakushukuru. (Makofi)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa mara ya kwanza swali langu hili limepata majibu mazuri ya Serikali, imenitia tumaini, lakini bado ina maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa sababu ya kituo hiki kuitwa kituo cha karibu cha usaidizi Mheshimiwa Waziri Mkuu alipokuja Liwale alituahidi kutujengea kituo kwenye Tarafa ya Kibutuka na Kata ya Lilombe. Je, ahadi hiyo itatekelezwa lini?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; kwa sababu jiografia ya Liwale kuwa ngumu hali ya usafiri ni mbaya sana, sasa je, Serikali iko tayari kutupatia gari kwa ajili ya maaskari wa kituo hiki?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, najibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kuchauka kwamba ahadi zote zilizoahidiwa na viongozi wa Serikali zitatekelezwa. Sasa hivi tupo kwenye kufanya tathmini kuona wapi paliahidiwa ili tuanze sasa utekelezaji wa ahadi hizo. Kwa hiyo hicho ambacho kimeahidiwa Mheshimiwa awe na amani kitatekelezwa.

Mheshimiwa Spika, kingine nimwambie ni kweli Serikali inafahamu umuhimu wa uwepo wa magari katika meneo mengi ambayo watu wanaishi kwa ajili ya kuhakikisha kwamba, kwanza tunafanya operation za mara kwa mara, lakini kufanya doria za mara kwa mara na kuhakikisha kwamba tunapambana na matukio ya kihalifu. Nimwambie tu Mheshimiwa kwamba katika gari ambazo zitafika tutahakikisha kwamba katika Jimbo la Liwale gari itakwenda ili iweze kusaidia wananchi kwa ajili ya kuweka hali ya amani na utulivu katika eneo hilo, nakushukuru.
MHE. PROF. PATRICK A. NDAKIDEMI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa fursa. Serikali imepeleka Polisi Kata kwenye kila Kata katika nchi hii kwenye rank ya inspector, lakini mapolisi hawa hawana ofisi wala makazi kwenye haya maeneo. Je, Serikali ina mpango gani kuwapelekea vijana wetu hawa kuwajengea Ofisi na nyumba za kuishi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, ni kweli tunatambua kwamba kuna baadhi ya Ofisi zimekuwa zimechakaa kwa sababu ni za muda mrefu, lakini vilevile tunatambua kwamba kuna maeneo mengine hata hizo Ofisi zinakuwa changamoto, lakini nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tutajitahidi, kama ambavyo tumejibu katika majibu yetu ya msingi, tutajitahidi kuhakikisha kwamba kila mahali wanapata Vituo vya Polisi, lakini kila mahali wanapata nyumba za makazi kwa ajili ya Askari Polisi, nakushukuru.
MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi niweze kuuliza swali dogo la nyongeza. Je, ni lini Serikali itawajengea askari polisi wa Wilaya ya Kilolo kwa sababu hawajawahi kujengewa nyumba, wanaishi kwenye nyumba za kupanga? (Makofi)

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeanza kutoa maibu yangu kwamba, tutahakikisha katika bajeti ambayo tumeeleza hapa katika jibu letu la msingi, tutahakikisha kwamba tunaanza ama tunaendeleza kujenga nyumba za makazi, kwa sababu kama tulivyosema mwanzo hiyo changamoto tunaifahamu na tunajua kwamba askari wetu wengi wanaishi kwenye nyumba nyingi zimechakaa, lakini tutahakikisha kwamba tunawajengea nyumba na makazi ya kisasa ili waweze kukaa kwenye makazi mazuri na kuweza kutoa huduma vizuri kwa wananchi.
MHE. MARYAM AZAN MWINYI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa majibu mazuri ya Serikali, nina maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa tayari Wizara imeshatunga katika kanuni na miongozo ya biashara ya hewa ukaa. Je, ni jitihada gani ya Wizara katika kutoa uelewa wa biashara hii kwa jamii hasa wanawake? (Makofi)

Swali langu la pili, je, Zanzibar inanufaika vipi kutokana na fedha inayotokana na faida ya biashara hii ya hewa ya ukaa? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, najibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Maryam pamoja na Wabunge wote kwa kuwa na hamu sana ya kutaka kujua faida na fursa mbalimbali ambazo zinapatikana kwenye biashara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, Zanzibar sasa muda wowote inakwenda kuanza kunufaika kutoka na biashara hii, tulichokuwa sasa tunakisubiria ni kwanza tunasubiri tumalize utafiti. Zanzibar tunayo misitu kwa upande wa Pemba tunao Msitu wa Ngezi lakini kwa upande wa Unguja tunao Msitu wa Jozani na kama unavyojua kwamba biashara hii inavunwa kwenye misitu hasa misitu ya asili. Kwa hiyo, tutakapokamilisha utafiti wetu Zanzibar inakwenda kunufaika kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa tulisema wacha tuendelee kutoa taaluma kwa wananchi hasa kwa upande wa Zanzibar, tumeshaanza kushirikiana idara ya mazingira tumeanza kutoa taaluma, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi tumeanza kuwapa taaluma. Kwa hiyo, muda wowote kuanzia sasa Zanzibar inakwenda kuanza kunufaika na biashara hii ya hewa ukaa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa jitihada ambazo zimechukuliwa ni kwamba, tumeunda kikosi kazi na kikosi kazi hichi kimekuwa kinashirikiana na TAMISEMI katika kuzunguka nchi yote kuhakikisha kwamba tunawafundisha wananchi. Tayari tumeshaanza kwenye baadhi ya Halmashauri za Mkoa wa Tabora, Simiyu, Katavi, Manyara na maeneo mengine. Kwa hiyo, taaluma hii tutahakikisha kwamba inaenea kote na juzi tulikuwa na Kamati za Wabunge kuwapa taaluma hii ya biashara ya hewa ukaa. Nakushukuru. (Makofi)
MHE. YAHAYA O. MASSARE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Pamoja na majibu mazuri ya Serikali, nina maswali madogo mawili ya nyongeza. Kwa kuwa wanyama hawa wamekuwa wanashambulia watu na tatizo ni upungufu wa Askari: Je, ni lini Serikali itaongeza askari katika Kituo cha Doroto ambacho ni Makao Makuu ya Game Reserve ya Muhesi?

Mheshimiwa Naibu Spika, swali la pili. Kuna waathirika wengi wamevamiwa, wengine wameuawa, mashamba yao yameliwa na tembo, au wanyama wakali wameuawa: Je, ni lini mtalipa watu wetu hawa katika Jimbo langu katika Halmashauri ya Itigi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Naibu Spika, najibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli tunakiri kwamba kuna upungufu wa askari ambao wanatakiwa walinde kwenye maeneo haya. Nimwambie tu Mheshimiwa kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, ndani ya mwezi huu tutahakikisha kwamba tunapeleka Askari katika kituo cha Doroto ili kuhakikisha kwamba shughuli za ulinzi wa wananchi dhidi ya wanyama wakali zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwambie tu kwamba tayari Serikali ya Mama Samia Suluhu Hassan imeshaachia kiasi cha shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuhakikisha kwamba wote walioathirika na athari za wanyamapori wakiwemo tembo wanapatiwa fidia zao na kupatiwa malipo yao, nakushukuru.
MHE. ESTHER E. MALLEKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana. Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la nyani na ngedere ambao wamekuwa ni waharibifu sana kwa mazao ya wananchi: Je, Serikali haioni sababu ya kuwahamisha au kuwauza nje ya nchi ili kujipatia fedha za kigeni? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Naibu Spika, moja ya miongoni mwa wanyamapori ambao tunawatumia sana kwa shughuli zetu za utalii na kivutio cha watalii kwa ajili ya kuingiza mapato katika nchi yetu ni hao kima na wengine. Hata ukiangalia kwa mfano kwa upande wa Zanzibar, kule kuna wale kima ambao nadhani dunia nzima wanapatikana tu Zanzibar. Kwa hiyo, kwa kusema kwamba tuwachukue tuwasafirishe nadhani hili tulichukue tuende tukalifanyie kazi tukafikirie zaidi. (Makofi)

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa nafasi ya kuuliza maswali mawili ya nyongeza. Kwa kuwa Wizara na taasisi zake zinatekeleza miradi hiyo moja kwa moja badala ya kupitia halmashauri.

Je, hawaoni sasa ni muda muafaka fedha hizo zitengwe zipelekwe halmashauri ili halmashauri itekeleze kwa usawia?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwenye Mkoa wa Kilimanjaro tumepitisha sheria kali sana za mazingira zinazozuia kukata miti kwa ajili ya kutunza mandhari ile na hali ya Mlima Kilimanjaro, jambo linaloleta usumbufu kupatikana kwa nishati ya kupikia kwa wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro.

Je, hatuoni sasa kwa Mkoa wa Kilimanjaro ni muda muafaka fedha hiyo ya CSR tuitumie kuwaletea wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro nishati mbadala ya bei nafuu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Tarimo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo ya fedha hizi ni kuhakikisha kwamba zinakwenda moja kwa moja kwenye community, kwa maana ya kwamba kwenye jamii. Hatuna shida na halmashauri lakini tumeona fedha hizi bora ziende moja kwa moja kutoka kwenye taasisi husika kwenda kwenye jamiii moja kwa moja kwa sababu kwanza tumeona jamii iweze kujua mchango wa uhifadhi na vipi wanaweza kunufaika na maeneo yale yaliyohifadhiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, cha pili tumeona kwamba, miradi mingi imekuwa inasuasua, sasa tukaona tukizipeleka fedha moja kwa moja, miradi hii itapata kumalizika kwa haraka na jamii iweze kunufaika. Kikubwa zaidi tumeona miradi ambayo inahitajika ndiyo iende kwa jamii. Kwa hiyo kikubwa nimwambie Mheshimiwa kwamba wazo lake sawa tunaweza kulichukua tukaona namna ya kulifanyia kazi, lakini kwa sasa tumeona bora fedha moja kwa moja ziende kwa jamii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine nimwambie kwamba, fedha hizi ziko kwa ajili ya miradi mbalimbali ikiwemo maji, umeme, zahanati na hata shule, lakini vile vile tu kwa kuwa sasa suala la nishati mbadala kwa sasa ni ajenda ya kitaifa, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba suala hili alilolishauri tunalichukua, tunakwenda kulifanyia kazi ili tuone namna ambavyo tunaweza tukachota fedha kutoka kwenye fungu hili na kuweza kushughulika na masuala ya nishati mbadala kwa sababu ndio ajenda ya Kitaifa, nakushukuru.
MHE. DENNIS L. LONDO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kuniruhusu kuuliza swali la nyongeza. Hifadhi za Taifa na Mapori ya Akiba imekuwa ni moja ya chanzo cha migogoro mikubwa kati ya wananchi na taasisi za Serikali, lakini kutokushirikisha wananchi kupitia sera hiyo ya uwajibikaji kwa jamii imekuwa ni moja ya vyanzo vya migogoro hii. Je, Serikali inaweza ikatoa tamko ni kwa nini fedha za CSR hazijaenda kwa wananchi ambao wanapakana na Hifadhi ya Mikumi kwa miaka sita mfululizo? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali hilo la nyongeza kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la fedha hizi ambazo kama ambavyo tumeeleza zinazotoka kwenye taasisi zinazosimamia uhifadhi. Lengo na madhumuni moja kwa moja ziende kwa wananchi, lakini changamoto iliyokuwepo ni moja kwamba fedha hizi haziwezi kutosheleza kupeleka kwenye Halmashauri zote kwenye maeneo yote. Kwa hiyo nimwambie tu Mheshimiwa, moja ni kwamba tunawashirikisha na ndiyo maana tukamjibu Mheshimiwa pale kwamba fedha hizi ni bora ziende moja kwa moja kwa wananchi ili tuwashirikishe na tuweze kujua wanachokitaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kikubwa nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutakapopata fedha, tutahakikisha kwamba kwenye Halmashauri yake na maeneo yake fedha hizi zinafika na zinatekeleza miradi ya wananchi.
MHE. JUMA USONGE HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nimpongeze sana Mheshimiwa Naibu Waziri kwa majibu mazuri ya utekelezaji wa CSR kupitia Halmashauri. Kwa ushauri wangu, je, Wizara sasa haioni haja ya kuja na sheria na kanuni kabisa ambazo zitawa-guide watu wa hifadhi pamoja na wanaofanya shughuli za kiutalii zaidi ili lile suala la CSR liwe suala la kisheria kabisa? Nashukuru.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wake tunauchukua na tutakwenda kuufanyia kazi. Nashukuru.

MHE. FRANCIS K. NDULANE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Je, ni lini Serikali itapeleka fedha za CSR katika Vijiji vinavyopakana na Pori la Akiba la Selous vya Zinga Kibaoni, Mtepela, Namatewa pamoja na Ngarambi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha katika Halmashauri hizo na maeneo aliyoyataja zitafika cha msingi Mheshimiwa Mbunge awe na subira, tutafute hizo fedha ili tuone namna ya kuja kusaidia wananchi katika maeneo hayo na wao waweze kunufaika na uhifadhi, nakushukuru.
MHE. SHALLY J. RAYMOND: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kuniona. Kwa kuwa waboreshaji wakubwa wa mazingira ni wanawake wakiwemo wanawake wa Kilimanjaro wnaaouzunguka mlima; na kwa kuwa hawa watu wanaotoa CSR wankwenda zaidi kwenye miradi mikubwa wakiacha kugawa miche na kuhakikisha kuwa miche ile inatunzwa na kuweza kufikia katika hali ya kurudisha uoto wa asili. Je, ni lini sasa taasisi hizo ikiwemo TFS wataweza kushirikiana na wanawake wa Kilimanjaro ambao wana nia sana ya kuboresha mazingira hayo kutokana na jambo alilolifanya Mheshimiwa Rais la Royal Tour kugawa miche ya matunda na miche ya kuboresha mazingira na kurejesha? (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA K.n.y. WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kwamba kuna uharibifu mkubwa wa mazingira maeneo hayo hasa yanayozunguka Mlima wa Kilimanjaro. Uharibifu ambao unasababishwa na shughuli za kibinadamu na hapa tunataka tuchukue fursa hii tutoe maelekezo tuwaambie wananchi, tuwashauri sana, waache kufanya shughuli za maendeleo katika maeneo haya zikiwemo za ufugaji na mambo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutajitahidi tupeleke fedha kwa Mkoa huu wa Kilimanjaro, hasa kwa akinamama, lengo na madhumuni ikiwa ni kuweza kurejesha ile hali katika ule Mlima Kilimanjaro. Nakushukuru.
MHE. KABULA E. SHITOBELA; Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kuwa Serikali imeshaandaa mkakati maalum wa kukabiliana na changamoto ya viumbe vamizi. Je, ni lini mkakati huu utaanza kufanya kazi rasmi?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Shitobela kuwa mkakati huu umeshaanza kufanya kazi na umeshaanza kufanya kazi takribani karibu miaka miwili nyuma iliyopita. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwa kushirikiana na Wizara nyingine za kisekta kama vile Wizara ya Maji, Wizara ya Kilimo lakini pia Wizara ya Mifugo na sisi Mazingira tumekuwa tukishirikiana kwa karibu sana.

Mheshimiwa Spika, kwanza tunashirikiana kwa ajili ya kutoa elimu na takribani vikundi 40 tumeshavipa taaluma namna bora ya kutumia ziwa hili na kupunguza huu ueneaji wa haya magugu maji.

Mheshimiwa Spika, kikubwa nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kutafuta fedha, lengo na madhumuni ikiwa ni kuhakikisha kwamba, tunapambana na hili jambo kwa sababu ni jambo ambalo Ziwa Victoria limeingiza nchi tatu au nchi nyingine.

Kwa hiyo, sisi huku tukiyakata kwa wenzetu yanaendelea kumea, kwa hiyo na mwisho wa siku yanarudi tena kwetu, lakini hata hivyo tunaendelea kupambana changamoto hii, nakushukuru.
MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kupata nafasi hii. Ziwa jipya lililoko Wilayani kwangu Mwanga mpakani na Kenya, upande wa Tanzania unakaribia kupotea kabisa kwa ajili ya magugu maji. Je, Serikali ina mpango gani wa kutekeleza ahadi yake ya kuondoa magugu maji katika Ziwa Jipe? Ahsante.
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, azma ya Serikali hii ni kuhakikisha kwamba tunaondosha changamoto zote zinazogusa kwenye eneo la mazingira ikiwemo changamoto ya kuenea kwa magugu maji. Nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kuzitafuta fedha kokote ziliko ili kuhakikisha kwamba tunaondoa magugu maji katika maeneo yote. Pia nimwambie kwamba siyo hili tu, yapo maziwa mengi yana changamoto hii. Hivyo, nimwambie tu kwamba hata katika Ziwa Jipe tutahakikisha tunakwenda kuondosha kabisa changamoto ya magugu maji, nakushukuru.

MHE. REGINA N. QWARAY: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kuniona; je, Serikali ina mpango gani wa kuokoa Ziwa Basutu ambalo kwa sasa linaonekana limejaa mchanga na kusababisha maji kusambaa kwenda kwenye makazi ya watu?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Ziwa hili limekuwa lina changamoto kubwa ya kuingia kwa mchanga ambao sasa unakwenda kuleta athari kubwa ya kimazingira. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge ni kwamba tumeshashirikiana na wenzetu wa halmashauri na baadhi ya taasisi nyingine kama ambavyo nimeanza kujibu awali, kuhakikisha kwamba kwanza tunaendelea kuwapa elimu wananchi, kwa sababu tuligundua kwamba changamoto hii ya uingiaji wa mchanga na hayo masuala ya magugu maji, mengi tukiwatizama changamoto za kimazingira zinasababishwa na wananchi wenyewe hasa kwenye shughuli zao za kibinadamu za kawaida. Nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba, awe na subra Serikali inakwenda kushughulikia hilo.
MHE. KAVEJURU E. FELIX: Mheshimiwa Spika, ahsante sana, Serikali ina mkakati gani wa kupambana na mimea vamizi nchi kavu na majini ikiwa Dodoma tayari tuna mmea vamizi ambao unaitwa Kongwa?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, moja miongoni mwa changamoto siziiti mpya, lakini miongoni mwa changamoto za kimazingira ambazo tuko nazo sasa hivi ni changamoto ya kuvamiwa na viumbe vamizi ikiwemo mimea na wadudu. Kwa hiyo, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, suala hili tumeliona na tumeshaanza kulifanyia utafiti kwa sababu tumegundua kuna baadhi ya mimea mingine ni vamizi lakini haina athari kimazingira. Kwa hiyo, kwa hii ambayo ni vamizi na ina athari kimazingira tutahakikisha kwamba tunakwenda kulishughulikia na tutalifanyia kazi katika mikoa yote kwa sababu siyo Dodoma tu hata mikoa mingine tumegundua ipo hiyo changamoto. (Makofi)

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Spika, nashukuru. Kwa kuwa suala la magugu maji limekuwa ni tatizo kubwa, ni kwa nini Serikali isifanye utafiti kuona kama kuna eneo ambalo magugu maji haya yanayotumika kama raw material ili yaweze kuvunwa kirahisi zaidi?

NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, jambo ambalo Mheshimiwa Mbunge amelishauri ni jambo jema na kwa sababu tumegundua kwamba hata nchi jirani wameshaanza hivyo na ndio maana unakuta changamoto ya kuenea kwa magugu maji inakuwa kubwa sababu sisi tukiyatoa, kwa wenzetu yanakuwepo na kwa sababu Ziwa ni moja yanarudi.

Mheshimiwa Spika, wenzetu Uganda wameshaanza kulifanyia hilo, wanatengeneza mikeka na mambo mengine na sisi tumo kwenye kufanya utafiti, nini ambacho tunaweza tukatengeneza. Nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba, tutahakikisha na sisi tunatumia magugu maji kama raw material kwa ajili ya kuinua vipato vya wananchi, nakushukuru.
MHE. ENG. STELLA M. MANYANYA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Mheshimiwa Jacqueline ana maswali mawili ya nyongeza.

Mheshimiwa Spika, swali la kwanza; je, Serikali ina mpango gani wa kutoa ruzuku kwenye nishati mbadala ikiwemo majiko ya gesi pamoja na gesi?

Mheshimiwa Spika, swali la pili; je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa maeneo yanayochimbwa madini kama makaa ya mawe pamoja na mchanga yanafukiwa au kurejeshwa katika hali yake ya asili kwa wakati na inavyostahili?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania alishiriki kwenye mjadala mmoja muhimu sana wa kitaifa ambao ulikuwa unazungumzia masuala ya kupunguza nishati ya matumizi ya kuni. Katika mjadala ule kuna maelekezo yalitoka tulipewa sisi Wizara tunaohusika na masuala ya mazingira na Wizara nyingine:-

(i) Tuendeleze kutoa elimu kwa wananachi;

(ii) Tunatakiwa tusimamie sheria, zipo Sheria za Mazingira; na

(iii) Tunatakiwa tuhamasishe wananchi wapande miti kwa wingi ili tuirejeshe miti ambayo ilishakatwa kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Spika, nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba jambo alilolishauri la kuhakikisha kwamba tunaweka ruzuku kwenye matumizi haya ya nishati hasa gesi na nishati nyingine, tutalichukua tunakwenda kulifanya kazi kuona namna ambavyo tunakwenda kuhamasisha zaidi wananchi katika masuala ya kutumia nishati bora ya kupikia instead of kutumia kuni.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, tayari tulishatoa maelekeza kwa wachimbaji wote wa madini au wachimbaji wote wa makaa ya mawe kuhakikisha kwamba mashimo wanayoyabakisha baada ya kuchimba wayafukie. Pia tulishatoa maelekezo kwa Mameneja wetu wote wa NEMC wahakikishe kwamba wanawapa taaluma na taaluma wameshapewa wachimbaji wote wa makaa ya mawe ili kuweza kuepuka athari kubwa ya mazingira ambayo inaweza ikajitokeza hapo mbele.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru.
MHE. JACQUELINE N. MSONGOZI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuuliza swali moja dogo la nyongeza lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, bajeti ya Serikali ya 2023/2024 imepanga kutoza asilimia 10 ya mapato ya mnufaika ambaye ni mkulima; kwa nini Serikali isisamehe tozo hiyo kwa wakulima wadogo ili kuwavutia wakulima hao kwenye kuwekeza zaidi kwenye uvunaji wa carbon?

Swali la pili, Mwongozo wa Carbon wa mwaka 2022 umejikita zaidi katika biashara za carbon za misitu mikubwa, lakini Serikali haimtambui mkulima huyu mdogo; je, Serikali itaboresha lini mwongozo huo ili biashara ya carbon kwa wakulima itambulike rasmi? Ahsante. (Makofi)
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwa kuanzia na swali la kwanza; suala la uwepo wa tozo ni suala ambalo lipo kisheria, lakini jambo la kusamehewa tozo ama kupunguza hiyo tozo pia lipo kisheria. Mimi nimwombe tu Mheshimiwa kwamba atupe muda twende tukakae na Wizara inayohusika, wakiwemo wenzetu Wizara ya Fedha, tuone namna ya kuweza kuzungumza nao ili lengo na madhumuni kuweza kuwapa nafasi wakulima wadogo wakaweza ku-invest zaidi kwenye carbon baada ya kupunguziwa tozo hiyo, kwa sababu biashara hii inalenga zaidi kule kwenye community.

Mheshimiwa Spika, swali la pili; nataka nimwambie Mheshimiwa Mbunge kwamba Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, juhudi ya kwanza ambayo tumeifanya ni kutengeneza kanuni na miongozo, jambo ambalo limeshakamilika. Lakini ni kweli tumeona na tumegundua kwamba kuna baadhi ya mapungufu, na sasa hivi ninavyozungumza tumeshaanza kuzifanyia review kanuni hizi. Hivi ninavyozungumza kuna timu yetu ipo Morogoro imekaa kwa ajili ya kufanya baadhi ya mapendekezo kuongeza vitu ili mradi tuweze kuwapa nafasi wakulima na wengine.

Mheshimiwa Spika, nimwambie tu Mheshimiwa Mbunge baada ya review hii tutaona maboresho makubwa yatakayokuja kugusa kwenye sekta za wakulima, sekta za wafugaji na sekta za wafanyabiashara. Nakushukuru.
MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Naomba niulize maswali mawili ya nyongeza. Swali la kwanza; kwa kuwa kata zote zilizotajwa hapo saba hazipo hata kata moja ambayo ipo kwenye Tarafa ya Chamriho; na kwa kuwa Tarafa ya Chamriho ina kata ya Nyamanguta, Nyamswa, Kitale, Salama, Bihingo, Mgeta na Unyali. Sasa ni lini Serikali itapeleka mradi huu ambao uko Bunda kwenye hizo kata alizotaja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili; kwa kuwa mradi huu unaelimisha watu juu ya madhara ya climatic change Serikali ina mkakati gani sasa wa kupeleka semina mbalimbali na warsha katika maeneo haya ili kuelimisha watu juu ya tabia nchi inayotokea kwenye maeneo haya?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu maswali mawili ya nyongeza ya Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika jibu la msingi ukiangalia kwenye paragraph ya pili imeonesha kwamba Serikali kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira, tunaendelea kufanya jitihada mbalimbali za kuhakikisha kwamba tunakaa na wadau na wafadhili mbalimbali ili kuweza kupata fedha twende tukaendeleze mradi huo katika hiyo Tarafa ya Chamriho. Kwa hiyo Mheshimiwa Mbunge aendelee kuwa na Subira, lakini pia kama kuna namna ya kufanya Halmashauri ya Wilaya ya Bunda watuandikie hilo andiko walilete kwetu Ofisi ya Makamu wa Rais, twende tukalipeleke kwa ajili ya kuliombea fedha ili tukakamilishe mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, swali la pili, miongoni mwa kazi yetu kubwa tunayoifanya katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuhifadhi mazingira ni kuchimba visima maeneo mbalimbali ili kunusuru hali hiyo. Kwa hiyo nimwambie tu kwamba tunakwenda kutafuta fedha ili twende tukachimbe visima ili kuweza angalau kuokoa maeneo hayo huku tukisubiria mradi huo uweze kukamilika. Nakushukuru.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza naomba nipongeze majibu mazuri sana ya Naibu Waziri. Hata hivyo, kwa heshima ya Mheshimiwa Boniphace Getere na nikifahamu kwamba ameendelea kuwapambania wananchi wake kwa nguvu kubwa sana. Ofisi yetu itafanya kila liwezekanalo mwanzoni mwa mwaka wa fedha katika eneo hilo tutatengeneza borehole moja ya mfano kama kuwafariji wananchi wa Kata ya Chamriho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni sambamba na maelekezo yaliyotolewa na Naibu Waziri katika majibu ya awali. Kwa hiyo, nimwambie Mheshimiwa Getere kwamba, tutakwenda kuchimba borehole ya haraka sana katika Kata ya Chamriho. Lengo letu ni kuanzia hapo kwanza wakati tukijadili mambo mengine, ahsante sana.
MHE. KHALIFA MOHAMED ISSA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa ya kuuliza swali dogo la nyongeza. Kisiwa cha Mtambwe Mkuu kilichopo katika Jimbo la Mtambwe, Pemba ni kisiwa ambacho kimeathirika sana na tabianchi, maji ya bahari yanaathiri sana makazi ya wananchi wasiopungua 500. Je, ni lini mradi huu wa climate change utawafikia watu wa Mtambwe Mkuu ili kunusuru kaya zao?
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Mohamed Issa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli tumeona hizo athari za kimazingira ambazo zimetokezea katika Kisiwa hicho cha Mtambwe Mkuu, lakini nimwambie kwamba aendelee kuwa na Subira, tupo kwenye michakato kuhakikisha kwamba maeneo yote ya visiwa ambayo yameathirika kutokana na shughuli mbalimbali za kibinadamu, tunaendelea kutengeneza mazingira ili angalau visiwa hivyo viweze kuwa salama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nataka nitoe wito, visiwa hivi vinakuwa vinapata athari za kimazingira kutokana na shughuli za kibinadamu, watu wanakata miti hasa mikoko, watu wanafanya shughuli za ujenzi lakini na mambo mengine. Kwa hiyo pamoja na kwamba Serikali tunaenda kufanya juhudi ya kukiokoa na kukinusuru kisiwa hiki lakini kwa ushirikiano wa Wabunge na viongozi wengine wa Serikali, tuendelee kuwaelimisha wananchi wetu ili sasa waone namna na umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwenye maeneo haya hasa maeneo ya visiwa.