Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Hamad Hassan Chande (6 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira
NAIBU WAZIRI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii ya kutoa mawili, matatu kwa zile hoja ambazo zimetolewa na Waheshimiwa Wabunge. Pia niwashukuru sana wale wote waliochangia katika mada hizi mbili, suala la Muungano na Mazingira kwenye Ofisi yetu. Nawashukuru sana kwa michango yenu mizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa muda siyo rafiki, naomba kwa ruhusa yako niende tu moja kwa moja kwa baadhi ya hoja ambazo zimetolewa na Wabunge, hasa kuhusu Muungano.

Mheshimiwa Spika, hoja ya kwanza ambayo imetolewa na Mheshimiwa Khadija Hassan Aboud; Muungano umetimiza miaka 57. Pongezi zimepokelewa. Aidha, Serikali ya SMZ na Serikali ya SMT zinaendelea na jitihada za kutatua changamoto kumi za Muungano zilizobakia ambazo 15 tayari zimeshapatiwa ufumbuzi.

Mheshimiwa Spika, hoja yake ya pili ni ushauri; ametoa ushauri kuhusu kuimarisha na kudumisha Muungano. Ushauri umepokelewa. Aidha, Serikali ya Awamu ya Sita chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan na Awamu ya Nane ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar chini ya uongozi wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mheshimiwa Dkt. Hussein Ali Hassan Mwinyi, zimeweka masuala hayo ya Muungano kwa nia moja vipaumbele vyake hivyo ni Serikali zote mbili kushirikiana katika kuzipatia ufumbuzi hizi kumi zilizobakia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hoja ambayo ameitoa Mheshimiwa Bakar Hamad Bakar kwamba kuenzi Muungano ni pamoja na kuwezesha viongozi wa Muungano huu, mfano Dkt. Omar Ali Juma; maoni yamepokelewa. Aidha, Serikali italifanyia kazi suala hili.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ameitoa Mheshimiwa Kassim Hassan Haji ni kuhusu Muungano wa Taasisi zetu za Zanzibar na zile za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kama vile TBS na ZBS kule Zanzibar. Suala hili ushauri huu tumeuchukua kwa mikono miwili na hatua zimeanza huko nyuma kwasababu mwenyewe nilikuwepo ZBS, tumeshakaa vikao tofauti, mbalimbali kujadili suala hili hapa. Kwa hiyo, ushauri umechukuliwa na tutaufanyia kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia ipo hoja ya Mheshimiwa Mwanakhamis Kassim Said ambaye hoja yake alikuwa anatoa pongezi, pongezi hizo zimechukuliwa na zimezingatiwa na tutazifanyia kazi kwa kadri inavyowezekana.

Hoja nyingine ya Mheshimiwa Mwanakhamis, haikuwa zaidi nayo ni pongezi tu kwa Jamhuri ya Muungano na kudumisha Muungano wetu wa Tanzania.

Mheshimiwa Asia Abdukarimu Halamga, Mbunge Viti Maalum, pongezi zimepokelewa na tutazifanyia kazi. Suala linaloshughulikiwa na kamati ya pamoja ya SMZ na ya SMT zinashughulikiwa masuala ya muungano baada ya kukamilika Serikali itatoa taarifa kuhusu jambo hilo.

Mheshimiwa Spika, ipo hoja ya Mheshimiwa Omar Ali Omar Hafidh, yeye amesema tu Elimu ya Juu, sana sana alizungumzia suala la mitaala kwamba hakuna mlingano mzuri kati ya mtaaala unaotumika Zanzibar na ambao unatumika Tanzania Bara. Suala hili tumelichukua na tutalifanyia kazi, tutafuatilia kwa kadri inavyowezekana ili tuweze kulinganisha mitaala yetu hiyo, ili kusudi tija na mafanikio ya wanafunzi wetu yawe yanalingana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya summary hiyo ambayo imetolewa na Waheshimiwa Wabunge katika Bunge lako hili Tukufu naomba tu niseme zipo changamoto kumi na tano ambazo zimeshapatiwa ufumbuzi na zimebakia changamoto kumi nazo kwa hakika karibuni kadri vikao vitakavyokaliwa na Serikali ufumbuzi wake utapatikana moja baada ya nyingine.

Mheshimiwa Spika, naomba nizungumze mambo mawili kuhusu muungano. Katika kipindi ambacho muungano unahitajiwa ama unahitajika zaidi Tanzania ni kipindi hiki. Hii ni kwasababu wapo maadui wengi wenye macho mabaya na makali wanaoutazama vibaya Muungano wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa hiyo, kipindi ambacho kinahitajika ni hiki, kwasababu hata wahenga wanasema Umoja ni Nguvu na Utengano ni Dhaifu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, na siku zote mbwa mwitu hula nyama ya kondoo aliyejitenga. Lakini jambo la pili, tuachane na wale watu ambao wana mawazo mgando ama fikra mgando kuhusu suala la muungano. Kwani hata ingekuwa ile tarehe 26 Aprili,1964 wangeulizwa kuhusu Muungano basi wangejibu hayo hayo kwamba kwao Muungano usingefaa.

Mheshimiwa Spika, naomba niombe kwa Waheshimiwa Wabunge na Wananchi kwa jumla, mambo mawili tu; jambo la kwanza, kwa kuwa wapo watu wenye ujauzito wa mawazo kuhusu Muungano naomba tuwe madaktari wazuri sana wakuwafanyia tiba, upasuaji, taratibu kabisa ili wajifungue salama, wawe wanajua nini dhana ya muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini jambo la pili, ambalo naomba ni wale watu wenye degree zao, maarifa yao makubwa ambayo maarifa hayo tunatarajia yabakie ndani ya ubongo wao lakini kwa bahati mbaya maarifa hayo wanayahamisha na kuyapeleka kwenye matumbo yao. Ili kusudi kubomoa mwelekeo wa Jamhuri ya Muungano. Naomba watu hawa tuwaelimishe na naamini wataelimika inshallah.

Mheshimiwa Spika, baada ya hayo naomba nitoe shukrani kubwa kwa familia yangu, ambayo tulikesha pamoja katika kuandaa haya. Lakini pili nitoe shukrani kubwa sana kwa wapiga kura wangu wa Jimbo la Kojani kwa kuniwezesha kufika hapa leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana, naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote nami nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu Rahim ambaye ametuwezesha kukutana katika Bunge hili na kujadili taarifa hizi tatu za Kamati zetu na bado anatupa thamani ya ubinadamu. Thamani ya ubinadamu ni uhai tu, ukiondoka uhai, basi tumekosa thamani ya ubinadamu na ndiyo maana tunaondolewa katika makazi ya watu na kupelekwa katika makazi maalum. Jambo la pili, naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama yetu Samia Suluhu Hassan, kwa namna anavyo pambana na kupigania kwa kujitoa kabisa kwa maslahi ya Taifa na wananchi wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba pia nikushukuru wewe kwa kunipa fursa hii na mimi kutoa mchango wangu katika mjadala huu, Mungu akubariki sana. Naomba niwashukuru Wenyeviti wa Kamati hizi tatu lakini na Wenyeviti wa Kamati zote, niwashukuru na niwapongeze sana Wabunge wenzangu ambao mmechangia na kwa kweli mchango unalenga kujenga Taifa letu. Michango yenu ni mizuri sana na kila mmoja ambaye amesimama hapa nilikuwa namuona anaongea, anatoa hoja kwa hisia kali sana, kwa uchungu wa nchi yake, nawashukuru na ninawapongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba moja kwa moja nijielekeze katika hoja ambazo zimeletwa na Waheshimiwa Wabunge. Nikianza na hoja ya mwenendo wa utoaji fedha kwenda LGS siyo mzuri, ametoa mfano Mheshimiwa Mbunge, Halmashauri ya Mwanga.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2021/2022 bajeti yao ilikuwa ni bilioni 2.31 kwa ajili ya kujenga miradi ya maendeleo ya Halmashauri hiyo ya Mwanga. Serikali ilitoa shilingi bilioni 5.07 sawa na asilimia 219 kupeleka ndani ya Halmashauri hiyo. Mwaka 2022/2023 bajeti yao ilikuwa Bilioni 5.55 hadi kufikia Oktoba tayari Serikali imeshatoa Bilioni 1.85 sawa na asilimia 33.74. Ofisi ya Msajili wa Hazina ipo katika mchakato wa kuboresha sheria ili kuonesha baadhi ya vipengele vyenye upungufu hususan utaratibu wa kutoa adhabu kwa baadhi ya viongozi wa Taasisi za Umma ambao wanakiuka taratibu na sheria.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ni ya GPSA. Kwanza naomba nikiri kwamba GPSA imechelewa au imechelewesha kutoa huduma hiyo ya magari. Kwa kweli, suala hili limechangiwa na sababu mbalimbali ikiwemo UVIKO–19 pia vita vya Ukraine, hii imechangia sana ucheleweshaji wa ununuzi wa magari hayo. Serikali imelipokea hili nikuhakikishie na nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba tutalichukulia hatua haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Spika, ipo hoja ambayo inasema Wizara ya Fedha na Mipango iboreshe mazingira ya Internal Auditors katika Serikali za Mitaa. Wizara ya Fedha na Mipango, tayari imepitia muundo wa Idara ya Internal Auditors na Mamlaka za Serikali za Mitaa…

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika taarifa!

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Jerry William Silaa.

T A A R I F A

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Spika, nimemsikiliza mchangiaji kwa makini na nimechelea kidogo. Nimemsikia akisema ziko hoja zimetolewa na Wabunge na anataka kutoa majibu, lakini hoja iliyoko mezani ni hoja ya Kamati za Bunge na Wabunge wote waliochangia wamechangia hoja ile na yeye kama mchangiaji ni vyema akachangia hoja ili tuweze kuihitimisha hoja. (Makofi)

SPIKA: Nafikiri kwa sababu hapo mwanzo alikuwa anaelezea utangulizi sasa anaenda kwenye hoja. Kwa hiyo, akishaanza hizo hoja ndiyo tutajua anazungumzia hoja za Kamati, kwa sababu pia Wabunge mmechangia humu ndani. Kwa hiyo, yeye yale yanayohusu Wizara yake ni muhimu ayatolee ufafanuzi. Kwa hiyo, mpaka tuanze kumsikia ndiyo tutajua kama ametoka nje ya hizi Kamati tatu na taarifa zake na je hilo jambo ambalo analolisema lilichangiwa humu ndani au hapana. Mheshimiwa Naibu Waziri karibu uendelee na mchango wako. (Makofi)

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa ruhusa hii. Naomba nitoe ufafanuzi kwenye hoja iliyotolewa na Bunge kuhusu mtaji wa Benki ya Kilimo ya Tanzania. Kwanza naomba nikiri kwamba ni kweli Serikali iliahidi kutoa mtaji wa kupeleka katika Benki ya Kilimo ya Tanzania lakini mpaka sasa imetoa Bilioni 60 kutokana na uchache au uhafifu wa bajeti tuliyokuwa nayo. Serikali ipo katika juhudi mbalimbali kuhakikisha kwamba imeongeza mtaji katika benki hiyo kwa maendeleo ya benki hiyo lakini wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, juhudi ambazo Serikali imechukua, kwanza Serikali imechukua mkopo nafuu wa Dola za Kimarekani Milioni 92.55 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika na kuikopesha TADB. Pili, Serikali imeamua kuifutia Benki ya Kilimo mkopo wa Dola za Marekeni 92.55, takribani Bilioni 216 na kugeuza kuwa mtaji wake ndani ya benki hiyo. Tatu, Serikali imechukua mkopo nafuu wa Euro Milioni 80 takribani Shilingi 185 kutoka Benki ya Maendeleo ya Ufaransa na kuikopesha benki hiyo. Hatua nyingine ambayo imechukuliwa na Serikali, ni Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu iliipatia Benki ya Maendeleo pesa takribani Dola za Kimarekani Milioni 25 kwa ajili ya dhamana kwa wakulima wadogo kutoka IFAD. Aidha, Serikali inaendelea kuangalia vyanzo vingine vya fedha ili kuipatia benki hiyo kwa maendeleo ya benki hiyo lakini na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ambayo ilizungumzwa na baadhi ya Wabunge ni kuhusu makinikia. Kwa mujibu wa taarifa ya CAG ya mwaka 2021 ukurasa wa 63, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali alibainisha kuwa baadhi ya mashauri ya kodi hususan yanayohusiana na sakata la makinikia yaliondolewa katika Mahakama za Rufaa za Kodi ili kushughulikiwa kwa utaratibu wa majadiliano kati ya Serikali na Kampuni za Madini. Katika majadiliano hayo Serikali ilijenga hoja na kufanikiwa kupata mafanikio haya yafuatayo: -

(i) Kulipwa Dola za Marekani Milioni 300, takribani Shilingi za Kitanzania Bilioni 700.

(ii) Kampuni ya Barrick kukubali kufuta kesi ya madai ya fidia kwa Serikali Dola za Marekani Bilioni 2.7.

(iii) Pia, kupewa umiliki wa asilimia 16 kwenye migodi ya kampuni hiyo ambapo imeunda kampuni mpya inayojulikana kwa jila la Twiga Mineral Cooperation. Barrick wao wana asilimia 84 na Serikali ina asilimia 16 katika hisa iyo.

(iv) Serikali imepokea jumla ya gawio la Dola za Marekani Milioni 36 na kupokea gawio kutokana na marekebisho ya mkopo kwa wanahisa. Dola za Marekani Milioni 16 kwa kipindi cha 2020/2021 na Barrick imekubali kutenga kiasi cha Dola za Marekani Sita kwa kila wakia kwa dhahabu zote ambayo itauzwa kwa ajili ya shughuli za kijamii.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huo, sakata la madai ya kodi ya Shilingi Trilioni 360 lilihitimishwa kwa Serikali kuridhia makubaliano haya kama ilivoainishwa katika maelezo ambayo ameyatowa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango katika Bunge lililopita.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingine ilikuwa ni malimbikizo ya madeni hasa TANROADS. Serikali imechukua juhudi kubwa sana, kwa sababu madeni haya Serikali ya Awamu ya Sita imeyarithi, lakini imechukuwa juhudi kubwa sana katika kulipa madeni hayo yaliyokuwepo na tunaendelea. Nilihakikishie Bunge lako Tukufu kwamba tutaendelea kulipa na miradi yote ambayo imeandaliwa na Serikali ya kimkakati basi itatekelezwa na tutalipa certificates hizo zikishaletwa kwa wakati kabisa.

Mheshimiwa Spika, ilikuwepo hoja ambayo imezungumzwa kuhusu utaratibu wa kufuta madeni chechefu katika benki zetu za TIB na TCB. Serikali imeshaanza kuchukua hatua za kuondoa madeni chechefu katika benki za TIB na TCB ambapo taratibu zinaendelea kuhakikisha madeni hayo yanaondolewa kwenye vitabu vya benki.

Mheshimiwa Spika, ipo hoja ambayo imezungumzwa kuhusu kukosekana kwa bodi kunasababisha mashirika kukosa umakini wa kufanya kazi. Serikali imeendelea kuweka juhudi katika kuhakikisha Taasisi na Mashirika ya Umma yanakuwa na Bodi za Wakurugenzi hai. Kwa sasa Serikali imeshafanya uteuzi wa Bodi za Wakurugenzi zipatazo 23 kati ya Bodi 31 ambazo zimesalia Bodi Nane na hizo Serikali inachukuliwa hatua katika kipindi kifupi kabisa Serikali itakuwa imefanya uteuzi wa Bodi hizo.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri hebu rejea hapo kwenye takwimu za Bodi.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kuweka juhudi katika kuhakikisha Taasisi na Mashirika ya Umma yanakuwa na na Bodi za Wakurugenzi hai, kwa sasa Serikali imeshafanya uteuzi wa Bodi za Wakurugenzi zipatazo 23 kati ya Bodi 31 ambazo zilikuwa hazina Bodi. Serikali inakamilisha utaratibu wa kuteua Bodi za Taasisi Nane zilizosalia…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nataka kumpa taarifa Mheshimiwa Naibu Waziri kwamba Bodi anazosema Serikali iko katika mpango wa kuteua Wajumbe wake kwa taarifa ya CAG, Bodi zingine zipo toka mwaka 2015, Serikali bado tu inaendeleaa na utaratibu wa Wakurugenzi wameshakuwa wamiliki wa hizo kampuni. Ahsante.(Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Hamadi Chande unapokea taarifa hiyo. (Kicheko)

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, nina ukakasi kidogo wa kupokea hiyo taarifa, lakini mimi niseme tu kwamba takwimu ambazo tunazo ni hizi 31 na 23 tumeshafanya uteuzi wa bodi, zilizosalia ni nane. Nadhani tuna asilimia zaidi ya 70, kwa hiyo awe na subira tu Mheshimiwa Mbunge ataona matokeo hivi karibuni, bodi zilizobakia tunateua. (Makofi)

SPIKA: Sasa Mheshimiwa Naibu Waziri, kwa sababu kwenye taarifa ya Kamati walitaja Bodi zaidi na ni sehemu ya maazimio ya Kamati. Mwenyekiti wa Kamati ambayo inazungumzia hizi Bodi ili tutakapofika kwenye maazimio tusianze tena kurejea nyuma. Mwenyekiti wa Kamati zile takwimu ulizonazo na hizi Bodi anazozitaja Mheshimiwa Naibu Waziri ni tofauti ni hizi au hili ni jambo jipya.

MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Spika, kuna tofauti kubwa sana. Taarifa tulizonazo kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina mpaka kufikia tarehe 31 Oktoba, jumla ya mashirika 23 hayana Bodi za Wakurugenzi. Kuna mashirika 12 ambayo tayari Mheshimiwa Rais ameshateua Wenyeviti wa Bodi lakini bado Wajumbe hawajateuliwa. Kwa hiyo, jumla ni mashirika 35 mpaka kufikia tarehe 31 Oktoba wakati tunaandaa taarifa hii mashirika hayo hayana Bodi.

SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri, hizi takwimu anazosema Mwenyekiti zipo sawasawa? Nataka tu kwenye takwimu ili wakati wa Azimio tusije tukaazimia na yale ambayo Serikali imeshayafanyia kazi.

Mheshimiwa Naibu Waziri, Mheshimiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma anasema Bodi 23 kufikia mwishoni mwa Oktoba zilikuwa hazina Wajumbe wala hazina Wenyeviti, Bodi 12 zina Wenyeviti ambao Rais ameshawateua lakini Wajumbe wale wanaoteuliwa na vyombo vingine ama na Mawaziri bado. Hizi takwimu zipo sawasawa?

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa swali hilo. Suala hili la Bodi ambazo tuko na uhakika nazo ni Bodi 23 ambazo Wajumbe wake wameshateuliwa na zimeshakamilka. Hizi nyingine labda zipo kwa upande wa Taasisi nyingine ama Wizara nyingine lakini mimi nazungumzia ambazo ziko ndani ya Wizara ya Fedha.

SPIKA: Hivi Treasury Register anaripoti wapi? Mheshimiwa Mwenyekiti Treasury Register anaripoti wapi? (Makofi)

SPIKA: Mwenyekiti, Treasurer Registrar anaripoti wapi?

MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Spika, Msajili wa Hazina anaripoti Wizara ya Fedha na Mipango. (Makofi)

SPIKA: sawa. Mheshimiwa Naibu Waziri, mimi nimekuelewa hoja yako. Ni kwamba hizi taasisi zinaweza kuwepo lakini kwa sasa hivi hapo hauna takwimu nazo, kwa hiyo sisi tutaendelea na azimio letu kuhusu hizi taasisi. Mheshimiwa Waziri wa Nchi anataka kutoa ufafanuzi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa sana ya kikao chako hiki cha Bunge, kwa spirit ambayo ameingia nayo Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, na hasa baada ya kukuta tatizo hili la teuzi za bodi kwamba ni tatizo ambalo limekuwa likijitokeza sana Serikalini; Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo na Chief Secretary na taasisi zinazohusika walishapewa kazi ya kusimamia.

Mheshimiwa Spika, itakuwa ni kumtendea haki Mheshimiwa Rais na kazi nzuri ambayo imekwishakufanywa kwani katika kipindi hiki…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Tabasam ngoja nijaribu kuelewa hoja kwanza kabla hujatoa taarifa yako, maana hajaanza bado kutoa hoja. Mheshimiwa Waziri wa Nchi.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Nadhani itakuwa ni vizuri kama katika kipindi hiki ambacho tunaelekea kuhitimisha hoja hii tukapata fursa ya kupata taarifa ambazo ziko kamili. Ninaheshimu taarifa za Mwenyekiti ambazo zimeishia mwezi Oktoba, lakini tangu mwezi Oktoba, mpaka sasa tunaweza kuwa na taarifa ambazo ni current.

Mheshimiwa Spika, kwa heshima kubwa sana, kama utaridhia, tuweze kupata taarifa hizo ambazo tunaweza kuzipata sasa hivi kutoka kwa Treasurer Registrar ili azimio letu tukishalipitisha hapa liwe ni azimio ambalo limebeba dhana kamili ya idadi kamili ambayo inatakiwa kuwasilishwa. (Makofi)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Sasa, kulikuwa na taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Tabasam, sijajua taarifa nyingine inatoka wapi. Sasa ngoja, kwa sababu mtapata fursa ya kuchangia, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI nawe ni kuhusu Bodi pengine zilizokuwa chini yako ambazo umezifanyia kazi kati ya huo muda. Sawa, Mheshimiwa Tabasam.

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, leo tupo serious na tumeamka vibaya, na ninaomba kabisa Waheshimiwa Mawaziri waje na nidhamu kabisa kwa siku ya leo, kwa sababu suala la vetting liko chini ya Ofisi ya Rais ambapo Waziri anayekuja kuzungumza maneno haya vetting iko kwake, na yeye ndiye sehemu ya ucheleweshaji wa vitu hivi. Tusubiri tufike mwisho leo. (Makofi)

SPIKA: Mwenyekiti nimekuona. Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, naona ulisimama.

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Spika, nami nilitaka kutoa tu taarifa; kwamba katika bodi tatu, sijajua taarifa ya Mwenyekiti wa Hesabu za Mashirika ya Umma au Uwekezaji katika Mashirika ya Umma kama na za kwetu zimo. Endapo zimo, kwa Bodi ya DART tayari imeshaundwa, kwa Bodi ya Masoko ya Kariakoo tayari imeshaundwa, na Bodi ya Mikopo ya Serikali za Mitaa pia nayo tayari tumeshaiunda, kwa hiyo kwa upande wangu wa TAMISEMI bodi zote tatu zipo.

SPIKA: Haya, ahsante sana. Mwenyekiti wa Kamati ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma, naona ulikuwa umesimama.

MHE. JERRY W. SILAA - MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA UWEKEZAJI WA MITAJI YA UMMA: Mheshimiwa Spika, naomba nitoe maelezo madogo kutokana na taarifa zilizotolewa hapa, na kwa kuwa jina la Mheshimiwa Rais limetajwa, naomba ninukuu Hotuba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, aliyoitoa tarehe 30, Machi 2022, nanukuu; “CAG umeeleza kuwa, mwenendo wa Mashirika ya Umma ambayo umebainisha Mashirika 38 ya Umma yanaendeshwa bila kuwa na Bodi. Hii inashangaza kwa miaka kadhaa mashirika yanaendeshwa hakuna Bodi za Wakurugenzi. Mimi nakumbuka nilipoingia nilipata mtiririko wa maombi ya bodi na yote nimeshayatoa. Sasa kama Waziri ana mashirika, bado anaendesha mashirika yasiyo na bodi, siwezi kumuelewa na sijui tatizo ni nini.” (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimesema niyaseme haya kwa sababu kuna mashirika ama kuna Wizara wakati mwingine zinatupa mzigo wa uteuzi kwa Mheshimiwa Rais, lakini Mheshimiwa Rais alishasema hadharani kwamba yeye anateua bodi kwa wakati, la kwanza.

Mheshimiwa Spika, lakini la pili, Ofisi ya Msajili wa Hazina inao mfumo ambao unatoa taarifa kwa Wizara miezi tisa kabla bodi haijamaliza muda wake ili mchakato na urasimu wote wa vetting ukamilike kwa wakati. Kwa hiyo tunaporipoti hapa, tunaripoti mambo ambayo tunauhakika nayo na yamethibitshwa na Ofisi ya Msajili wa Hazina na yako sahihi, na kwa nyongeza, tarehe 30, Oktoba ni siku nne kuanzia sasa ndiyo taarifa yetu imetoka.

SPIKA: Haya, ahsante sana. Mheshimiwa Naibu Waziri wa Fedha na Mipango, malizia mchango wako.

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipatia tena fursa hii. Nimalizie mchango wangu kwa hoja iliyokuwa inazungumzia Sheria ya Manunuzi kwamba ina upungufu.

Mheshimiwa Spika, hili nikiri kwamba sheria hii ina upungufu; na kama alivyoeleza Mwanasheria Mkuu wa Serikali hatua ambayo imefikiwa kwa sasa ya kufanya marekebisho ya sheria hiyo iko katika ngazi ya maamuzi na karibuni hivi itaingia Bungeni kwa ajili ya kupata mapendekezo na maoni kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge. kwa hiyo niwatoe wasiwasi Waheshimiwa Wabunge kwamba suala la Sheria ya Manunuzi na sura 410 lipo katika hatua ya maamuzi kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, wapo wachangiaji wengi ambao walichangia kuhusu manunuzi. Kwamba kuna upotevu mkubwa sana wa fedha katika manunuzi. Naweza kusema kwamba zaidi ya asilimia 70 ya fedha za bajeti za Serikali zipo katika manunuzi. Kwa hiyo hii ni sehemu moja nyeti na muhimu sana na Serikali imeichukulia hatua sehemu hii kwa kiasi kikubwa sana. Kutokana na mapungufu yaliyokuwepo pale, Serikali imeamua kuanzisha mfumo mpya wa manunuzi ambao unaitwa NEST ili kuepuka changamoto ambazo zinajitokeza wakati wa kufanya manunuzi.

Mheshimiwa Spika, na hii yote ni kwa sababu ya mfumo tulio nao si rafiki kwa matumizi ya watumiaji na pia utoaji wa taarifa sahihi. Kwa hiyo tumeamua Serikali kuanzisha mfumo huu, na faida ambazo zinaweza kupatikana kutokana na mfumo wa sasa wa NEST ni nyingi sana. Kwa mfano, itaongeza uwazi (transparency) kwa sababu mfumo uliokuwepo usiri ulikuwa ni mkubwa sana ambao unaweza kupelekea mianya ya rushwa. Mfumo huu utakuwa uko wazi na watumiaji wote watakuwa wana-access.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, utaongeza uwajibikaji; kutakuwa na uwajibikaji mkubwa sana katika mfumo huu. Faida nyingine ambayo inaweza kupatikana katika mfumo huu ni kuweka ukomo wa bei za bidhaa, yaani kuweka bei kikomo au bei elekezi, kwamba bidhaa hii bei yake ni hii hapa ili kusudi kuepuka manunuzi holela. Maana inawezekana bidhaa moja hii mfano ya kalamu kwa idara tofauti zikawa na bei tofauti kutokana na mfumo ambao ulikuwepo, lakini kwa sasa mfumo huu unaenda kujenga na kutuweka wazi. Na huu ndiyo mwarobaini pekee wa ku-save fedha za Watanzania.

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Deus Sangu, Mheshimiwa Naibu Waziri.

T A A R I F A

MHE. DEUS C. SANGU: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana; naomba kumpa taarifa mzungumzaji. Mfumo huu wa TANEPS ambao upo sasa ni mfumo ambao umewekwa hivi karibuni, mwaka 2020 ndio ulikuwa mandatory kwa taasisi zote za umma na umegharimu mabilioni ya fedha za Watanzania. Leo hii ndani ya miaka miwili Serikali yenyewe iliyoweka huo mfumo inatuambia kwamba ni redundant na hauna maana, na wanatuambia wanakuja na mfumo wa NEST ambao uta- address matatizo haya. Hivi kweli huu sio ufisadi mwingine? (Makofi)

SPIKA: Mheshimiwa Sangu kwa kawaida taarifa huwa haina maswali lakini, Mheshimiwa Naibu Waziri wa fedha na mipango unaipokea taarifa hiyo?

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, hii taarifa siipokei kwa sababu unaweza kuishi na mke hata kwa siku tatu tu; bila kujali gharama ya mahari uliyotoa; ukaona kwa mwenendo huu sasa huyu hanifai tena. Kwa hiyo unaweza kuacha. Hata kama umetumia siku tatu, achilia miaka miwili. Kwa hiyo taarifa hii mimi siipokei.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu tunaotarajia kuutumia endapo utatumika, kwa utafiti mdogo ambao tumeufanya, utakoa zaidi ya shilingi trilioni mbili. Pia mfumo huu utawezesha Ripoti ya Mkaguzi Mkuu wa Serikali angalau kuwa na matokeo mazuri badala ya kuwa na matokeo hasi siku zote, kwa sababu tunakwenda kujadili na kuona wapi kuna mwanya au kuna viashiria vya upotevu wa fedha kabla mradi haujaanza, tofauti na mfumo ambao ulikuwepo.

Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kutoa wito kwa taasisi zote za Serikali kujiunga na mfumo huu ambao utasaidia matumizi halali. Ahsate sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma (PIC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kunipa fursa hii lakini awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu Rahimu ambaye amepitisha mjadala huu katika hali nzuri na usimamizi wako mzuri kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niungane na wenzangu kushukuru sana kwa kuchaguliwa kuwa Naibu Spika wa Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Niwapongeze pia watoa hoja wenyeviti wote wawili ambao yaani Mwenyekiti wa bajeti na mwenyekiti wa PAC ambao wamewasilisha ripoti zao hapa au taarifa zao ziko vizuri niwapongeze sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhamira ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni kupunguza mzigo kwa wananchi wake wa Tanzania, dhamira hiyo inaendelea katika kuonekana utekelezaji wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hasa katika suala ambalo hoja imezungumzwa ama maoni yametolewa na kamati ya bajeti kuhusu riba. Naomba niongelee hapo kwamba Serikali inachukua hatua mbalimbali katika kupunguza mzigo kwa wananchi wake hasa wale wakopaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuagiza sekta ya bank na taasisi ya fedha kuweka mikakati ya kupunguza gharama za uendeshaji ikiwemo kuhamasisha matumizi ya teknolojia katika kutoa huduma za fedha kwa lengo la kupunguzia mzigo mteja na kuhakikisha viwango vya riba vinashuka kufikia tarakimu moja tu yaani single digit.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kupitia benki kuu inatoa taaluma kwa wateja mbalimbali au kwa wananchi mbalimbali ili kududi wawe na maamuzi sahihi wakati wa kuingia katika mikopo hiyo. Serikali kupitia Benki Kuu ya Tanzania inaendelea kuchukua hatua mbalimbali kutatua changamoto na miongoni mwa hatua hizo mwezi Julai, 2021 hatua kadhaa zimechukuliwa ikiwa ni pamoja na kutoa unafuu wa kisheria katika kiasi cha amana ambacho bank na taasisi ya fedha zinatakiwa kuweka benki.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pili kurekebisha kauli za usajili wakala wa benki kwa kuondoa sharti la kuwa na uzoefu wa miezi 18 katika eneo la biashara, jambo la tatu kupunguza kiwango cha riba kinachotolewa kinachotolewa katika account za wateja watoa huduma za fedha kwa njia za simu za mkononi. Lakini benki imechukua hatua ya kuhakikisha benki kuu imeanzisha mfuko maalum wa shilingi trioni moja kwa riba ya asilimia 3 kwa mwaka. Benki Kuu imepunguza kiwango cha mtaji kinachotakiwa kuweka na benki za biashara kwa ajili ya kuweza kutoa mikopo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhakikisha kuwa uwiano wa gharama za uwendeshaji na mapato ya benki kuzidi asilimia 55 na mikopo chechefu isiyozidi asilimia 5, kushirikiana na umoja wa mabenki katika kusimamia maadili ya watendaji, kushirikiana mabenki pamoja na taasisi ya fedha, kufanya ukaguzi maalumu kwa wastaafu yote haya ni matarajio yetu kwa muendelezo huo zote hizi zitasaidia kuendelea kupungua kwa riba za mikopo nchini. Hivi karibuni tumeshuhudia benki kubwa za kibiashara zikipunguza riba kutoka asilimia 20 hadi asilimia 9 katika sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu pendekezo la kuanzisha Ofisi ya kupokea malalamiko ya kodi mapendekezo haya pia tumeyachukua kwa sababu pendekezo la muundo wa Taasisi ya kanuni za uwendeshaji zimeandaliwa tayari na zimekwisha andaliwa na kupelekwa kwa ofisi ya Rais Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala bora kwa evening, tunatarajia hivi karibu kabla ya kumalizika mwaka huu wa fedha itakuwa idhini hiyo tumeshaipa na muundo utaanza kutekelezwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba tu nijielekeze katika hoja ya pili ambayo imetokewa na Kamati ya PIC ambayo inazungumzia miradi kutokamilika kwa wakati. Serikali inatekeleza bajeti kama ilivyoidhinishwa na Bunge hadi kufikia mwezi Disemba, 2021 kiasi cha shilingi bilioni 585.1 zimetolea kwa ajili ya kugharamia miradi ya maendeleo sawa na asilimia 86.2 ya lengo nunu mwaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za maendeleo zilizotolewa zinajumuisha shilingi bilioni 5194.3 na fedha za ndani ni shilingi bilioni 167.1 fedha za nje. Aidha shilingi bilioni 443.7 ni fedha za washirika wa maendeleo zilizopelekwa moja kwa moja ya utekelezaji wa miradi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Kudhibiti Utakatishaji wa Fedha Haramu wa Mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa hii ili niweke neno katika michango ya Muswada huu. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu Rahhim ambaye ametuwezesha kukutana hapa na kufanya mjadala huu tukiwa katika hali ya uzima na afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, kwa dhati kabisa naomba kuishukuru sana Kamati ya Bajeti, sana kwa sababu, nimejifunza mengi. Vile vile nawashukuru sana Wabunge wenzangu kwa mijadala yao ya kujenga. Kila mmoja ambaye ametoa maoni yake yalikuwa ni maoni mazuri ambayo yanajenga katika maendeleo ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba nimshukuru sana Waziri wa Fedha na Mipango, kwa ushirikiano wake wa karibu sana nami katika utendaji na utumishi wa Serikali yetu. Namshukuru pia Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa michango yake na ushirikiano wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba niende tu moja kwa moja sasa kwenye baadhi ya michango ambayo imetolewa na Wabunge. Baadhi ya Wabunge wamechangia suala zima la kutoa elimu kwa wadau kuhusu Muswada huu. Kwa kweli hili niliseme kwa niaba ya Waziri kwamba tunalichukua na tutajitahidi kutoa taaluma kwa wadau wote ambao wanahusika na tunaahidi kwamba elimu hii itafika mpaka chini kwa wananchi wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, Mheshimiwa Kakunda ametoa maoni, amesema kwamba tuwe na kampeni maalum ya kuongeza uelewa kwa wananchi nalo hili pia tumelichukua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote tuwe Walimu wa kutoa taaluma kwa wananchi wetu juu ya sheria hii endapo itapitishwa, kwa sababu, madhara ya utakatishaji wa fedha haramu ni makubwa sana na ni hatari kabisa kwa maendeleo ya Taifa letu. Nawaomba sana Wabunge wenzangu, tuwe mstari wa mbele katika kutoa taaluma. Mwisho kabisa nawaomba Wabunge kupitisha Muswada huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. HAMAD HASSAN CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mtu wa awali katika wachangiaji kwa jioni hii ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, namshukuru Mwenyezi Mungu Subhanah-wataala ambaye ametuwezesha sisi kufika katika jengo hili na ametujalia kuwa na rasilimali ya uhai ambayo ndiyo inatoa thamani ya ubinadamu. Maana yake bila rasilimali ya uhai, basi binadamu anakosa thamani ya ubinadamu. Ushahidi wa hilo, moja kati ya sisi akipoteza uhai tu, basi wapenzi wake wa karibu ikiwemo familia yake, wanakaa kwa pamoja vikao tofauti kujadili wapi wanaenda kumweka na kumtoa kwenye nyumba hata kama ni nzuri aliyoijenga kwa gharama kubwa. Kwa hiyo, tumshukuru Mungu kutujalia rasilimali hii ya uhai. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu, nakishukuru sana Chama changu Cha Mapinduzi kwa kunipa nafasi hii, kuniteua tangu awali mpaka kufika hapa leo, kwa sababu ni chama makini chenye viongozi imara sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya shukurani hizo, naomba kwa ruhusa yako nianze na neno la Mungu kutoka katika Kitabu cha Qurani aya ya nane, Sura ya 102 inayosema:

Kisha kwa hakika mtaulizwa siku hiyo juu ya neema mlizopewa, mmezitumiaje? Kwa hakika tumepewa neema nyingi sana. Mungu ametujalia neema nyingi sana katika nchi yetu ya Tanzania pande zote, sisi ni wa kujivunia kwa neema hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu mimi ni Mbunge kutoka Jimbo la Kojani na Wakojani tunajulikana sana kwa shughuli za uvuvi, naomba tu nijielekeze huko kwenye masuala ya uvuvi. Neema hizi ambazo ametupa Mungu hasa katika suala la uvuvi baharini na hata kwenye maziwa, zipo kanuni ambazo zimewekwa na baadhi ya watendaji wetu wa Wizara ama Idara ambazo zimekuwa vikwazo vya kutumia vizuri neema hizo.

Kwa mfano, Kanuni ya 58A(1) na (2) inayomtaka mvuvi lazima atumie mtego wenye urefu wa mita 144. Hiki ni kikwazo kikubwa sana kwa wavuvi wetu, inayotaka uvue samaki wa sentimeta 26. Kwa kweli baadhi ya samaki ambao wala hatuharibu mazingira, tunawahitaji kuwapata, lakini inakuwa ni ngumu sana kwa wavuvi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni ya pili ambayo ni kikwazo kidogo ni 58A ya uvuvi wa dagaa. Inataka dagaa wanaovuliwa wawe ni wa sentimeta tano. Kwa kweli dagaa wa sentimeta tano hadi saba, unaweza ukamwita sio dagaa tena huyo, anaweza kuwa ni samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kanuni ya 66(1)(hh), taa za utumiaji katika uvuvi wakati wa usiku. Kanuni inataka taa ziwe ni za watts 50. Ni mwanga mdogo sana unaopatikana hasa kwa jiografia kwa baadhi ya maziwa kama vile Tanganyika au Bahari Kuu. Kuvua kwa watts 50 ni ndogo sana, samaki au dagaa hawezi kushawishika kuja katika mwanga na kuweza kumvua kwa urahisi. Kwa hiyo, ni vyema angalau iwe inafikia watts 200 au 300 kama kawaida ambavyo tunavua sisi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kanuni nyingine ambayo ni kikwazo ni ile inayomtaka mvuvi asivue wakati wa mbalamwezi, lazima avue mwezi unapokuwa giza. Sasa hizi sisi wavuvi kwa mfano wa ring net ambao tunavua usiku wote ikiwa ni wa mbalamwezi au wa giza, ukisema tuvue msimu huo, ukifika wakati wa mbalamwezi tukale wapi jamani? Au tusubiri mpaka uingie usiku mwingine wa giza, siku 15 zile, au siku 10; nadhani hiki ni kikwazo kikubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ubaya wa kanuni hizi, zinawafanya wavuvi wetu kutoroka katika nchi yetu na kwenda nchi za jirani. Baya zaidi, sisi tunafuga samaki, tunawalea, wanakua, wenzetu wa jirani ndio wanavua na kutumia samaki hao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu kwa hili ni kwamba, hizi kanuni zitakapowekwa au zitakapotungwa ni vyema kuwashirikisha na wavuvi, sio wataalam wa uvuvi peke yao ambao wanajisomea tu kwenye meza na viti. Walengwe kabisa wavuvi wenyewe kusudi washiriki kikamilifu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo nashauri kwa kuwa ni wa mwanzo nilinde kidogo; kanuni hizi zisiwe uzi wa buibui. Nadhani unaujua; spider yule. Kanuni hizi zilikuwa zinamnasa yule mdogo tu, kama vile uzi wa buibui, akipita kurumbiza, inzi, kipepeo, wanakamatwa na ule uzi; lakini akipita njiwa tu, anaondoka nao uzi wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakusudia kusema kwamba kanuni hizi zinapowekwa na idara zetu ni vyema ziwe zinakamata wale wakubwa na wadogo. Siyo wadogo tu ambao wanakamatwa hatimaye nyavu zao kuchomwa moto, tukasababisha watu kukataliwa majumbani kwao, tukaongeza idadi ya wajane na vijana wanaotelekezwa.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Hamad.

MHE. HAMAD HASSAN CHANDE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na naunga mkono hoja. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali za Fedha wa Mwaka 2022
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Awali ya yote naomba nimshukuru Mwenyezi Mungu Rahimu ambaye ametuwezesha kuwepo hapa tangu asubuhi hadi sasa tukiwa katika hali ya uzima na afya pamoja na amani.

Mheshimiwa Spika, pili naomba nikushukuru sana kwa kunipa fursa hii nami kuwa sehemu ya wachangiaji katika hoja hii iliyoko mezani.

Mheshimiwa Spika, nimshukuru pia Waziri wangu, Waziri wa Fedha na Mipango kwa namna anavyonisaidia na kunielekeza. Lakini pili nimshukuru Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti pamoja na makamu wake na wajumbe wote wa kamati husika nawashukuru sana kwa ushirikiano, maoni na maelekezo yao. Kwa ujumla niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa usharikiano wao wanaotuonesha ndani ya Bunge hili Tukufu.

Mheshimiwa Spika, mimi niende tu moja kwa moja katika mambo mawili ambayo kwa ujumla ni maoni ambayo yametolewa na Waheshimiwa Wabunge. Maoni haya yote yapo kwa lengo la kujenga Taifa letu na kwa maslahi ya Serikali yetu na wananchi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, maoni ambayo yametolewa na Kamati pamoja na wachingiaji moja ni usimamizi na ufuatiliaji wa matumizi ya Serikali. Hili niseme kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango tumelipokea na tutalifanyia kazi kwa maslahi ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Spika, jambo la pili ni kufanya tathmini ya kina katika misamaha yote ambayo inatolewa na Serikali kwa miradi mahiri. Nalo hili tunalichukua na tunaahidi kwamba Serikali italifanyia kazi kwa nguvu zake zote.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi hii. (Makofi)