Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Anton Albert Mwantona (5 total)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kupata nafasi kuweza kuongea neno kidogo kwenye Wizara hii ya Maji. Pia namshukuru Mungu kwa kunipa uhai hadi siku ya leo napochangia katika Wizara hii. Nampongeza sana Waziri wa Maji mdogo wangu Mheshimiwa Aweso, Naibu Waziri wa Maji Mheshimiwa Maryprisca Mahundi, Katibu Mkuu pamoja na watendaji wote wa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa, nimepitia bajeti ya Wizara ya Maji kwa kweli nimeona bajeti hii ni ndogo kwa Wizara hii. Mwaka huu wa fedha Wizara imepata shilingi bilioni 705 kwenye bajeti lakini kwa bahati mbaya sana fedha ambazo zimekuja kwenye Wizara ni bilioni 346 ambazo ni asilimia 53, ni fedha ndogo sana kwa Wizara. Tuombe Serikali ihakikishe kwamba fedha zinazopangwa kwenye bajeti zinapelekwa kama inavyotakiwa ili kumaliza kiu ya Watanzania kuhusu maji safi na salama kwa wananchi wake. Vinginevyo kila mwaka tutakuwa tunakuja kupiga kelele hapa kwamba bajeti ni ndogo, fedha haziendi na kwa sababu ya ufinyu wa bajeti ndio maana Wizara inashindwa kutekeleza malengo yake kama inavyotakiwa. Chonde chonde Serikali tunaomba tupeleke fedha kama inavyotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ninamshukuru Rais wetu, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alisema ataboresha Mfuko wa Maji nchini. Nimuombe Rais ahakikishe kwamba Mfuko wa Maji unapatiwa fedha ya kutosha ili changamoto za maji ziweze kuondoka hapa kwetu nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, nije Jimboni kwangu, namshukuru Waziri wa Maji pamoja na Naibu Waziri walipanga ziara kuja katika Jimbo la Rungwe wakatembelea miradi mbalimbali ikiwepo Mji wa Tukuyu, tukawaeleza matatizo yetu pale, mpaka leo local radio za pale Rungwe zimemnukuu Naibu Waziri akiahidi kwamba tatizo la maji Tukuyu litakwisha, kila siku ndio salamu za asubuhi pale Rungwe. Nashukuru Waziri Mheshimiwa Jumaa Aweso pamoja na Naibu Waziri baada ya kusikia kilio cha wana Rungwe, Mji wa Tukuyu juzi juzi wamewapelekea shilingi milioni 500.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia alitembelea Mradi wa Rukata, Kata ya Kinyala, juzi juzi pia kawapelekea shilingi milioni 100 angalau mradi uanze wananchi wapate moyo. Mheshimiwa Waziri pamoja na Naibu Waziri ninawashukuru sana Mungu awatie nguvu katika utendaji kazi wenu ili miradi hii ya wananchi iweze kwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi mwingine ambao napenda kuishukuru Wizara ni wa Masoko. Kuna mradi upo pale na kuna vijiji vingi vimenufaika. Kwenye bajeti hii kuna fedha kwenda kurekebisha madhaifu yalikuwepo kwenye mradi huu. Vijiji vitakavyofaidika nii zaidi ya 16 ambayo ni Ikama, Itagata, Lufumbi, Lupando, Bujesi, Lwifwa, Isabula, Mmbaka, Busisya, Burongwe, Ngaseke, Igembe, Mtandabara, Nsyasya, Mperwangwasi pamoja na Nsaga. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli hivi vijiji vilikuwa na matatizo makubwa, chanzo cha maji kimetokea katika eneo lao lakini maji ya kutosheleza yalikuwa hayapatikani katika vijiji hivyo. Wizara imetenga zaidi ya shilingi milioni 500 kwenda kurekebisha miundombinu ili wananchi katika maeneo hayo waweze kupata maji ya uhakika, hiyo peke yake nashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia Wizara imetenga fedha kwa ajili ya kupeleka maji kwa awamu ya pili katika mradi huu, vijiji 15 vinanufaika. Kuna Kijiji cha Mpumburi ambacho ni chanzo cha maji pia pale kinakwenda kupata maji. Vijiji vingine vya Segera, Mpombo, Masukuru, Ijiga, Mpakani, Byebe, Njugiro, Kiroba, Kikore, Matwebe, Kiambambembe, Lubanda, Katunduru na Ilima vinakwenda kupata maji. Hiyo ni shukrani ya pekee sana kwa Waziri lakini pia wa Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna vijiji vilikuwa kwenye bajeti ya mwaka huu ambayo inaisha mwezi wa sita, sijaviona kwenye bajeti inayofuata. Naomba chonde chonde tuna siku kadhaa kumaliza mwaka huu, mwaka unakwisha mwezi wa sita; kuna vijiji kama Champandapanda, Kata ya Kiwila mwaka huu unakwisha na ilitengewa shilingi milioni 205, kuna Kijiji cha Ikuti, Lyenje vilitengewa shilingi milioni 126, ni fedha ndogo, naomba Wizara kama kutakuwa na uwezekano kabla ya mwaka huu wa fedha haujaisha tuwapelekee hawa watu fedha ili miradi yao iweze kutekelezwa kwa sababu changamoto ni kubwa.

NAIBU SPIKA: Kengele imeshagongwa Mheshimiwa.

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano pale Lyenje pale Ikuti kuna kituo cha afya kimejengwa lakini kwa bahati mbaya sana hawana maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja, naomba kuwasilisha. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nashukuru sana kwa kunipatia nafasi nami kuchangia katika Hotuba hii ya Bajeti ya mwaka 2021/2022 katika Bunge lako Tukufu. Pili, namshukuru Mwenyezi Mungu kutupatia afya ili nami niweze kuchangia katika hotuba hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaongea kwa kifupi sana. Kwanza nianze kutoa shukrani zangu za dhati kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nilipokuwa nakwenda kwa mara ya kwanza kwenye kampeni, nimezunguka kwenye vijiji vyote 99 vya Rungwe, nimezunguka kwenye kata 29 zote za Rungwe, matatizo makubwa ya wananchi katika Jimbo langu ilikuwa ni barabara, maji, umeme na matatizo mengine madogo madogo. Matatizo makubwa ambayo wale wananchi walikuwa wakiniambia ukienda Bungeni ukatusemee ilikuwa ni hayo makubwa matatu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwanza na barabara za vijijini. Tumerekebisha Mfuko wa TARURA, Serikali imerekebisha; tunakwenda kupata shilingi 100/= kwenye mafuta, kwa hiyo, tatizo la barabara nina uhakika linaenda kutatuliwa na hivyo kunirahisishia mimi maisha kama Mbunge wa Jimbo, kuwaambia na kuwanyooshea vidole kwamba Serikali yetu imefanya mambo haya, haya na haya. Pia nashukuru kwa kiasi kikubwa, kwa shilingi milioni 500 ambayo imepatikana kwa kila Jimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kampeni zangu nilizunguka nikakuta kuna kijiji ambacho hakina barabara ya kuunganisha. Nilipanda pikipiki mpaka kwenda kupiga kampeni kwenye Kijiji hicho; kinaitwa Kijiji cha Kikole. Ni kilometa 12 kutoka kwenye mji ambao unapitika unaitwa Masukuru mpaka Kikole mpakani na Kyela. Napenda kulitaarifu Bunge lako Tukufu hili kwamba hiyo fedha tumeielekeza huko na wananchi wa Kikole niwaambie, mama amesikia kilio chenu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba amesikia kilio chenu na Serikali ya Chama cha Mapinduzi imesikia kilio chenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru sana Serikali, namshukuru sana Waziri wa Fedha, nashukuru sana Baraza la Mawaziri ambalo limefikiria kupeleka hii shilingi milioni 500 kwenda kuwasaidia wananchi katika maeneo ambayo yapo katika taabu kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa maji, pia tulikuwa na tatizo kubwa katika mji wetu mkuu pale Tukuyu katika Jimbo letu la Rungwe, lakini Serikali pia ilituletea shilingi milioni 500 mwezi uliopita na miradi mbalimbali inaendelea kutekelezwa katika Jimbo hilo. Wananchi wamefurahi sana na wanasema Mwantona tupelekee salamu kwamba wameiamini Serikali ya Chama cha Mapinduzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa umeme, sisi tuna vijiji 99. Vijiji ambavyo vilikuwa na umeme ilikuwa ni vijiji 66 na vijiji 33 vilikuwa havina umeme. Niwaambie wananchi wa Jimbo la Rungwe kwamba vijiji vyote 36 kwa mujibu wa bajeti hii, vinakwenda kupata umeme na wananchi wanaenda kufurahia matunda ya uhuru wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nitakuwa mchoyo wa fadhila kama sitashukuru Wizara ya Ardhi ambayo imekwenda kupunguza tozo au kiasi cha premium ambayo ilikuwa inalipwa katika upimaji wa viwanja vipya. Wametoa kutoka asilimia 2.5 hadi 0.5; lakini pia kwenye uhalalishaji wametoa kutoka 1% hadi 0.5%. Naona kabisa kwamba tunapokwenda, wananchi wengi watapima ardhi kwa sababu gharama imepungua, itakuwa ni ukombozi katika maisha yao kwa sababu ardhi ni mwanzo wa kujipatia mitaji na kufanya biashara zao ambazo zitawasaidia katika maisha yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hiyo ni shukrani pekee pia. Vile vile nashukuru kwa bajeti hii imekwenda kuangalia Property Tax. Nilimsikia mama kipindi fulani anasema kwamba tutumie akili zaidi kuliko kutumia nguvu katika ukusanyaji wa kodi za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme mbele ya Bunge lako Tukufu kwamba Waziri wa Fedha ametumia akili zaidi katika ukusanyaji wa Property Tax kuliko ilivyokuwa hapo awali. Kodi hii inakwenda kuongeza walipa kodi wengi zaidi (tax base) wanakwenda kuongezeka. Pia gharama za ukusanyaji wa kodi zinakwenda kupungua. Mara ya kwanza tulikuwa tunatumia Watendaji wa Kata, watu mbalimbali walikuwa wanaenda katika maeneo mbalimbali, gharama zilikuwa kubwa, lakini kwa kutumia utaratibu ambao umeshawekwa, gharama za ukusanyaji wa kodi zitapungua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niseme tu wazi kwamba kama kuna changamoto ambazo zipo, zishughulikiwe lakini utaratibu huu ni mzuri ambazo utasaidia sana kukuza mapato ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaomba nitoe ushauri kidogo kwa Serikali na nitaomba Waziri wa Fedha anisikilize especially kwenye halmashauri zetu. Halmashauri zetu ukiangalia kuanzia mwaka 2016/2017, 2017/2018, 2018/2019, 2019/2020 uwezo wa kujitegemea kwa halmashauri zetu uko chini 2016/2017 halmashauri ilikuwa na uwezo wa kujitegemea halmashauri zote kwa wastani ilikuwa ni asilimia 11, 2017/2018 uwezo wa halmashauri zetu kujitegemea nchini ulikuwa ni asilimia 13, 2018/2019 uwezo wa halmashauri zetu kujitegemea nchini kote ilikuwa ni asilimia 15 na mwaka huu kwa mujibu wa taarifa ya CAG uwezo wa halmashauri zetu kujitegemea umefikia asilimia 15 ina maanisha nini? inamaanisha kwamba mapato ya ndani ya halmashauri ukagawanya na matumizi mengineyo pamoja na mishahara ndiyo uwezo wa halmashauri kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa niseme kwa dhati kabisa kama Serikali yetu ya Chama cha Mapinduzi ambayo ni sikivu waangalie kwa jinsi gani kubadilisha mindset kuziwezesha halmashauri zetu kuongeza uwezo wa kujitegemea. Si vizuri sana kuonekana kwamba Serikali Kuu inaongeza uwezo wa halmashauri kutokujitegemea ili tuweze kuwasaidia tumekuja Wabunge wote hapa tumeshangilia sana madiwani wetu kupewa posho zao tumeshangilia sana watendaji wa kata kupewa posho zao. Lakini nishauri kwa Serikali yangu tukufu kwamba tuwasaidie halmashauri zetu kuendeleza kukusanya mapato kuliko kuwapelekea pesa kwa ajili ya kuwalipa madiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naweza nikatoa mfano mmoja tu ambao unaweza ukasaidia kuongeza mapato ya halmashauri service levy ambayo ni mapato makubwa sana chanzo kikubwa halmashauri zetu haikusanyi sheria ya fedha Local Government Finance Act ya Mwaka 1982 ambayo imekuwa advanced 2002 inasema kabisa kwamba halmashauri itakusanya service levy kwa mtu yeyote ambaye ana leseni ya biashara yoyote lakini utafiti mdogo nilioufanya halmashauri nyingi hazikusanyi service levy mtu yeyote mwenye biashara ana leseni ya biashara anatakiwa alipe service levy lakini hawalipi na ndiyo maana unakuta mapato ya halmashauri yanakuwa chini na hivyo uwezo wa kujitegemea unazidi kushuka mwaka hadi mwaka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tufanye utafiti kwenye service levy tuzisaidie halmashauri zetu ziweze kukusanya service levy ili kuongeza mapato yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona niliseme hilo kwa sababu siyo picha nzuri sana kwa Serikali kuonekana halmashauri nyingi sana zinategemea Serikali Kuu kuendesha shughuli zake siyo picha nzuri sana financial statement tunazidi kuzi-spoil za halmashauri. Kwa mfano nimeangalia haraka haraka hapa kwenye taarifa ya CAG kuna majiji yetu Matano. Jiji la kwanza ambalo liliongoza lilikuwa na uwezo mzuri wa kujitegemea lilikuwa ni Jiji la Dar es Salaam ambalo limeshavunjwa lilikuwa na asilimia 484 walikuwa na mapato ya bilioni 16 wakapokea mapato kutoka Serikali Kuu bilioni 3.6 ilikuwa ni milioni 484 ilikuwa ni asilimia 484 uwezo wake wa kujitegemea ulikuwa siyo mbaya ni mzuri lakini jiji la pili ilikuwa ni Dodoma walikuwa na asilimia 45 ya kujitegemea, jiji la tatu ilikuwa ni Arusha walikuwa na asilimia 32 ya kujitegemea. Jiji la nne ilikuwa ni Mbeya asilimia 20 ya kujitegemea Jiji la tano na la mwisho ilikuwa ni Tanga asilimia 6 ya kujitegemea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tusione fahari sana sisi kama Serikali kuwawezesha kuwapelekea hela za ruzuku kwenye halmashauri vinginevyo tuwatafutie mapato mengine ambayo yatawasaidia wao kuwawezesha kwenye financial statement zao kwamba uwezo wao wa kujitegemea unazidi kupanda mwaka hadi mwaka.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Anton ahsante.

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nami pia nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya aliyotupatia. Pia nimshukuru Rais wangu, Rais mpendwa Samia Suluhu Hassan kwa yale ambayo anatufanyia kwenye Majimbo yetu. Nimshukuru mdogo wangu Waziri Mheshimiwa Bashungwa, Manaibu wake Mheshimiwa Silinde pamoja na Mheshimiwa Dugange, nimshukuru pia Katibu Mkuu wa Wizara hii Shemdoe Profesa. Vile vile pia nimshukuru sana sana Engineer ambaye ni Mkurugenzi wa TARURA Ndugu Seif, lakini pia kwa namna ya pekee sana nimshukuru Engineer wangu ambaye yuko kule Jimboni kwangu au Wilayani kwetu Rungwe ambaye anaitwa Kamara, anafanya kazi kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, leo kwa sehemu kubwa nitakuwa nashukuru maeneo mengi, lakini nitakuwa na changamoto moja au mbili ambazo naomba Waziri ambaye ni Waziri makini sana aweze kusikiliza kwa makini na aweze kunisaidia katika Jimbo langu la Rungwe. Kwanza nashukuru sana kwa kupandisha bajeti ya Mfuko wa Jimbo kwa asilimia 45. Mfuko wa Jimbo una mchango mkubwa sana kwa maendeleo katika Majimbo yetu. Kwa hivi nashukuru sana kwa kupandisha hii bajeti kwa asilimia 45, ila nashauri kwamba hizi pesa za Mfuko wa Jimbo zifike mapema zaidi kwenye majimbo yetu kwa sababu ni muhimu kuchoche maendeleo kule Majimbo.

Mheshimiwa Spika, pia kwa sababu pesa itaongezeka, naomba hizi pesa zije hata kwa awamu mbili, ije awamu ya kwanza mwezi wa Saba, lakini baada ya miezi sita hizi pesa ziweze kuja tena kuchochea maendeleo. Kwa sababu muda mwingi utakuta unakaa mwaka mzima hizi pesa zinakuja mara moja kwa mwaka kiasi kwamba wananchi wanasahau kwamba kuna vitu vingine vinatakiwa kufanyika. Naomba Mheshimiwa Waziri alichukue hilo, kwamba tuangalie kama tunaweza kupata hizi pesa kwa awamu mbili katika majimbo yetu ili majimbo yaweze kuchangamka mara kwa mara.

Mheshimiwa Spika, suala lingine la pili, nimeangalia kwenye utekelezaji wa bajeti ya mwaka jana kwenye TAMISEMI bado mapato ya ndani kwenye halmashauri zetu siyo mazuri sana. Mwaka jana nilisema na mwaka huu naongea tenah kuna chanzo kimoja cha mapato katika halmashauri zetu ambacho kipo very potential na kama tutakisimamia vizuri tunaweza tukaongeza mapato katika halmashauri zetu. Chanzo hicho ni service levy, service levy inakusanywa inafanana na Sheria ya TRA ambayo ni kodi ya mapato.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kama tukishirikiana na TRA vizuri, tukafanya assessment, TRA wanafanya assessment zao na service levy wakafanya assessment kwa pamoja kama parallel tunaweza tukaongeza mapato kiasi kikubwa sana kwenye service levy na tukaongeza mapato ya Halmashauri zetu kwa kiasi kikubwa.

Naomba hilo lizingatiwe na Waziri aweze kuli-note, washirikiane na TRA kuhakikisha wanapo-produce zile assessments za TRA kwenye kodi ya mapato wa-produce pia assessments za service levy katika halmashauri zetu ili kuongeza mapato katika halmashari zetu.

Mheshimiwa Spika, suala lingine ambalo natoa pongezi kwa Wizara ni kuanzia mfumo wa kielektroniki katika kusimamia Mifuko ya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu. Hilo nawapa pongezi, naomba wakalisimamie kwa karibu kuhakikisha kwamba mambo yanayofanyika katika halmashauri zetu katika ngazi za TAMISEMI pia wanaweza wakayaona na wanaweza wakayashauri.

Mheshimiwa Spika, naomba niende kwenye afya. Mwaka huu wa fedha tumeletewa zaidi ya milioni 500 kwa ajili ya kujenga Kituo cha Afya Kiponjora, tumeletewa milioni 250 kwa pesa za tozo tunajenga Kituo cha Afya Ndanto, lakini tumeletewa bilioni 1.39 katika Hospitali yetu ya Wilaya Rungwe ambayo inaitwa Makandana. Milioni 300 ujenzi unaendelea, ilikuwa ni kwa ajili ya jengo la emergency, milioni 90 ujenzi unaendelea kwa ajili ya jengo la wafanyakazi, lakini bilioni moja kwa ajili ya ukarabati na ujenzi wa majengo pale katika hospitali yetu.

Mheshimiwa Spika, nilivyokwenda kwenye kampeni mwaka uliopita walinisisitiza sana na walinitwisha jiwe kichwani ambalo linasema kuna matatizo makubwa ya kiutendaji katika Hospitali yetu ya Wilaya. Haya ni lazima niyaseme kwa sababu ni mwakilishi wa wananchi, matatizo ambayo nayapata katika maeneo yao lazima niyalete hapa Bungeni.

Mheshimiwa Spika, Naibu Shaka Abdul Shaka ambaye ni Mwenezi Taifa alikuja kutembelea pale kwetu, alitembelea kata tatu, alitembelea Kata ya Kiwira, Bagamoyo na Mpuguso, matatizo yote anayoelezwa ni matatizo ya service ya pale katika Hospitali ya Wilaya ya Rungwe. Kuna matatizo makubwa sana, mimi mwenyewe nimefanya ziara kwenda kushukuru kwa wananchi, akinamama ndiyo waathirika wakubwa na wengine wanaambiwa kabisa kwamba bwana nenda ukamwambie Mama Samia hapa hatuna madawa.

Mheshimiwa Spika, tunajua kuna matatizo MSD, tumeambiwa hapa Bungeni, lakini kuna lugha za kuwajibu wananchi, ili tuwaambie wajue kwamba Serikali inapitia matatizo fulani ambayo tunayajua MSD kuna shida. Nampongeza Mheshimiwa Rais kwamba amebadilisha Mwenyekiti pamoja na Mkurugenzi MSD, hiyo napongeza sana kwa sababu tunategemea huko mbele ya safari tunapokwenda, tunakwenda kufanya marekebisho katika huduma zinazopatikana katika hospitali zetu.

Mheshimiwa Spika, naomba niseme tu kwamba kama hatutafanya marekebisho katika huduma zinazotolewa katika hospitali zetu nchi nzima, majengo tunayojenga ni bure, hayatatusaidia chochote, lakini kuboresha majengo na miundombinu mbalimbali inayofanyika katika hospitali zetu kwenye maeneo mbalimbali ni lazima yaende na elimu kwa watumishi wetu, tuwaambie wanatakiwa watoe service inavyotakiwa wananchi waweze kunufaika na matunda ambayo tunayapeleka katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, nasema hivyo kwa sababu, wananchi watamlaumu bure Mheshimiwa Rais kwa sababu tu kwamba tunajenga majengo lakini hakuna service inayopatikana.

Kwa hiyo, naomba sana sana Waziri Mheshimiwa Bashungwa nafikiri nimeshamwona, waende wakafanye marekebisho kwenye Hospitali ya Wilaya ya Rungwe, tupate huduma zinazotakiwa kwa wananchi wa pale Rungwe ili tuondoe malalamiko ya wananchi ambapo kila siku wanalalamika kwamba huduma zinazopatikana hapa hazitoshelezi.

Mheshimiwa Spika, nimalizie upande wa barabara. Nimempongeza…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza ni mimi nashukuru kwa kupata nafasi ya kuchangia mpango wa bajeti katika Wizara hii ya TAMISEMI. Nishukuru na nimpongeze sana Waziri wa TAMISEMI Mheshimiwa Angellah Kairuki, Naibu Waziri wake Mheshimiwa Ndejembi pamoja na Mheshimiwa Dugange, Katibu Mkuu na wote walio katika Wizara hii ya TAMISEMI wametengeneza bajeti nzuri ambayo
inaenda kutatua matatizo ya wananchi katika ngazi za chini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili niseme wazi kwamba namshukuru sana Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Biblia inasema kila jambo lina wakati wake. Kipindi hiki ni cha Mama Samia na yuko tayari kuwasaidia Watanzania kutatua matatizo yao mbalimbali ambayo yanatukabili kwa muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na TARURA nampongeza sana Mkurugenzi wa TARURA pamoja na Injinia ambaye amewekwa kule chini kijana wangu mmoja anaitwa Kamara anatusaidia sana kutatua matatizo ya barabara katika maeneo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme wazi kwamba kuna barabara ambazo zilikuwa hazipitiki miaka na miaka; kuna barabara ya kutoka Maskulu mpaka Kikole. Hii barabara iliwekewa jiwe la msingi na kipindi kile alikuwa anaitwa Salim Mohamed Salim, lakini kwa bahati mbaya hii barabara haikutengenezwa. Mama Samia ameingia madarakani tumeletewa milioni 473 barabara kutoka Maskulu mpaka Kikole imetengenezwa na wananchi kule wanafurahia matunda ya uhuru wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia barabara ya kutoka Kapugi kuelekea Lienje, pia ilikuwa ni barabara ya miaka mingi haikutengenezwa; lakini Mama Samia ametuletea pesa zaidi ya milioni 270 barabara imetengenezwa na sasa iko katika hali nzuri wananchi wanafurahia matunda ya uhuru wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengi sana katika barabara. Mimi wakati naingia kama Mbunge kuna barabara zaidi ya nne zilikuwa hazipitiki kabisa lakini leo ni barabara moja tu ambayo imebaki ambayo ni kutoka namba one pale Idweri kuelekea Ngumbulu. Namwomba sana Waziri aliangalie hilo kwa sababu ni barabara pekee ambayo imebaki ambayo kwa sasa hivi upitaji wake umekuwa ni mgumu, tuwasaidie pia wananchi wa Idweri kuelekea Ngumbulu ili barabara ile pia ipitike kwa muda wote wananchi waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika TARURA ninayo changamoto kidogo, Rungwe ni wilaya ambayo ina mvua nyingi. Tuna mtandao wa barabara zaidi ya kilometa 1,300 tuna mvua za kutosha, barabara nyingi zinaharibika lakini bajeti yetu ambayo tunapata ni zaidi ya shilingi bilioni 2. 5 ambayo ni ndogo sana kwa Rungwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba kama kuna uwezekano formula ya ugawaji wa fedha za barabara iweze kuangaliwa upya kwa sababu Rungwe ni kubwa lakini kipato tunachopata bado hakitoshelezi katika utendaji wetu wa kazi. Kwa hiyo, naomba hiyo tuliangalie tuone ni jinsi gani, pia hata fedha zinazopatikana za barabara kwa sababu ya hali ya hewa ya Rungwe ziweze kuletwa mapema katika maeneo yetu, zitumike mapema kwa sababu ikishaanza mvua tu utekelezaji wa barabara unakuwa tayari ni shida kubwa katika Jimbo langu la Rungwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa afya mwaka jana tulipata na ninamshukuru sana Mheshimiwa Rais tumepata vituo Vitatu vya afya Bilioni 1.5. Tulipata Kituo cha Ipojora, tulipata kituo cha Ndanto, tulipata kituo pia cha Kiimo ambavyo vyote vimeishakamilika na vifaa tiba vimeishakuja. Wananchi wanamshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwamba kazi sasa imeishaanza kufanyika na wananchi pale wanapata matibabu karibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeangalia bajeti ya mwaka huu pia tumepata vituo viwili vya afya, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwamba tumeletewa pesa Bilioni Moja ambayo itaenda kutusaidia wananchi wa Rungwe kuweza kupata huduma kwa karibu katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika hospitali yetu ya Wilaya tumepewa bilioni moja kumalizia jengo la OPD pamoja na Wodi kwa ajili ya wagonjwa zaidi ya 90, pia tunashukuru sana katika hilo kwamba Serikali imetufikilia kutusaidia katika kazi hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa elimu...

MWENYEKITI: Mheshimiwa ahsante sana kengele ya pili imelia, tunaendelea na Mheshimiwa...

MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa ahsante, naunga mkono hoja. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. ANTON A. MWANTONA: Mheshimiwa Spika, nami pia niungane na wenzangu kumshukuru Mungu kwa kutupatia afya, lakini pia nimshukuru Rais wetu mama Samia Suluhu Hassan, Waziri wa Fedha, Naibu wake na watumishi wote wa Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kutoa shukrani za pekee, wananchi wangu wameniambia nije nitoe shukrani kwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa miradi inayotekelezwa katika Jimbo langu la Rungwe. Ni miradi mingi inatekelezwa, lakini kwa upekee sana naomba nitaje miradi michache kwa sababu ya muda ili wananchi wangu wasikie kwamba nimewafikishia salamu zao.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Rungwe pamoja na mimi mwenyewe tumefurahi sana hasa baada ya Serikali kusikia kilio chetu, Mbunge mimi wa Rungwe wa Kyela, lakini pia Wabunge wa Viti Maalum dada zangu pale wa Mbeya tulivyokuwa tunapigania Mradi wa Makaa ya Mawe wa Kiwira. Serikali imeshapata mteja ambaye atanunua makaa ya mawe kutoka Kiwira tani 60 kila mwezi. Upatikanaji wa mteja huyo utatusaidia sana watu wa Rungwe, Kyela, Ileje kupata ajira lakini pia kupata uchumi katika maeneo yetu. Vijana wengi ambao wako katika maeneo yetu walikuwa hawana ajira, tunategemea kwamba baada mradi huu kuanza ajira nyingi zitapatikana katika maeneo yetu na vijana wengi wataajiriwa.

Mheshimiwa Spika, pia wameniambia nilete salamu na shukrani pekee kwa Mradi wa Maji katika Mji wetu wa Tukuyu kwa Wizara ya Maji, tumepewa juzi milioni 402 kufikia bilioni moja na milioni 102 ambapo mradi mzima una bilioni 4.5. Sasa hivi tutapata mabomba ya kutosheleza kutoka moja kwa moja katika chanzo mpaka Tukuyu Mjini. Kwa hiyo tuna uhakika sasa hivi maji yatapatikana ndani ya muda mfupi, hiyo ni shukrani ya pekee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tatu, katika bajeti hii tumewekewa milioni 90 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu kwa barabara inayotoka Kimo kuelekea Iponjola, Ikuti mpaka Ileje. Wananchi pia wanashukuru sana kwamba hii barabara ni dalili njema, kwamba inaanza kujengwa barabara hii kwa kiwango cha lami kutoka pale Kimo – Iponjola - Ikuti mpaka Ileje, hiyo ni shukrani ya pekee pia kwa Serikali hii.

Mheshimiwa Spika, pia kwa upande wa TARURA tumepewa tayari milioni 880 kwa barabara ambayo ilikuwa ni sumbufu sana kutoka Kijiji cha Kata ya Malindo, Kijiji Kapugi, kuelekea Lienje mpaka Kihobo Juu kwenye Kata ya Ikuti. Hizo ni shukrani za pekee sana kwa Serikali hii kwamba ni sikivu lakini pia imewafikiria wananchi kutatua matatizo yao ambayo yapo katika maeneo yetu.

Mheshimiwa Spika, niongee kidogo kwenye bajeti hii ya 2022/2023, nikipongeza Serikali kuongeza bajeti kwenye upande wa kilimo. Ongezeko ni kubwa ambalo litaenda kufanya mapinduzi makubwa kwenye kilimo. Mwaka jana tumepata shida kubwa sana kwa wananchi, tulivyokuwa tunafanya mikutano katika maeneo mbalimbali ya wananchi wetu tulikuwa tunaulizwa sana kuhusu bei ya mbolea. Bei ya mbolea kwa wastani laki moja mpaka laki moja na arobaini na hiyo imepelekea mwaka huu kilimo kikawa kigumu, watu wachache ndio waliweza kulima na hivyo tunategemea mwaka huu mazao yatakuwa ni kidogo.

Mheshimiwa Spika, katika suala hili naomba niishauri Serikali kwamba, tudhibiti chakula hicho kidogo tulichokipata, tuhakikishe kwamba utoaji wa chakula chetu cha nje kinatoka katika hali ambayo ni nzuri tukizingatia hasa usalama wa chakula hapa nchini. Hilo nimeona niseme, lakini kwa mwaka huu sasa kwa sababu tumeweka ruzuku kwenye mbolea uwezekano mkubwa ni kwamba mbolea itashuka na wananchi wengi watalima na hivyo tutapata chakula kingi cha kutosha.

Mheshimiwa Spika, Rungwe ni wafugaji wakubwa sana wa ng’ombe wa kisasa, tunafanya zero grazing, tunafugia ng’ombe ndani katika mazizi kwa kuwaletea chakula ndani, lakini tatizo kubwa la Rungwe na maeneo mengine ambayo wanafanya utaratibu huo wa ufugaji ni kwamba bei ya maziwa ni ndogo kwa wafugaji wetu. Tunaomba Serikali iangalie kwa jinsi gani itaongeza thamani ya mazao ya maziwa, lakini pia kuongeza soko mazao ya maziwa katika maeneo yetu. Rungwe ukifuga ng’ombe, lazima utumie lita 100 kununua mfuko mmoja wa pumba, pumba wanauza shilingi 70, maziwa yanauzwa kwa Sh.600 mpaka Sh.650. Sasa ukiangalia, kwa kweli wananchi wanapata shida, wanafuga mifugo yao katika gharama za juu lakini bei za maziwa ziko chini, kwa hivyo inawakatisha tamaa wengi katika ufugaji wao.

Mheshimiwa Spika, niende katika Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani. Mheshimiwa Waziri amesema hapa kwamba Kitengo cha Ukaguzi wa Ndani kinaongezewa independence zaidi kwa kupewa vote yao, lakini pia kwamba wao watakuwa wanaripoti moja kwa moja kwa Internal Auditor General ili at least zile ripoti zao ziweze kwenda vizuri na zisiingiliwe na mtu yoyote, ni jambo jema. Hata hivyo, naomba tuangalie pia katika utaalam wa kihasibu kwa sababu Internal Auditor ni sehemu ya menejimenti ya taasisi husika.

Mheshimiwa Spika, hapo lazima tuangalie jinsi gani ya kutenganisha Internal Auditor Unit lakini na kule anakoenda kuripoti, tusije tukatengeneza ugomvi mkubwa zaidi, halafu mambo yakazidi kuwa mabaya, kwa sababu Internal Audit kazi yake kubwa ni kushauri hiyo taasisi ambayo ipo ili kuhakikisha kwamba internal control ya taasisi inakaa vizuri na hakuna matatizo yoyote ambayo yanaweza kutokea kama mambo ya wizi na kadhalika. Kwa hiyo tuweze kuangalia vizuri hapo, ni jambo jema kuanza kutenganisha hapo.

Mheshimiwa Spika, mwisho niongelee watumishi ambao Mheshimiwa Waziri amesema kama wakiondolewa kwenye madaraka yao, kama alikuwa ni Mkuu wa Taasisi, tuchukulie labda ni Mkurugenzi, akiondolewa kwenye nafasi yake anatakiwa aende akatumikie mshahara wake ule wa awali, kama alikuwa ni Mtendaji wa Kata akachukue mshahara wake wa Mtendaji Kata. Naona hili kwangu sikubaliani nalo.

Mheshimiwa Spika, nashauri Serikali waangalie upya katika hili kwa sababu tutakuwa tunawaonea watu wengi sana, kwa sababu watu wengi ukiangalia kutokana na historia wanaondolewa katika sehemu zao za kazi bila kuzingatia utaratibu. Anaweza akaja Mkuu wa Mkoa, akaja Mkuu wa Wilaya akamsimamisha mtu kazi kwa muda miaka sita, miaka saba, lakini hapati haki zake, anakuja mtu mwingine anachukua nafasi yake anachukua ule mshahara, halafu unasema kwamba tunamrudisha kwenye mshahara wake wa kipindi cha nyuma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba tuzingatie sheria iliyopo, kama tunataka kuanzisha sheria nyingine ambayo itawafanya watu wapunguziwe mishahara yao, basi tuanze sasa hivi lakini ajira basi ziwe za mikataba kama ajira zingine, lakini si ajira zile ambazo mtu anapewa barua ya ajira inakuwa ni permanent and pensionable lakini wanamwambia kwamba arudi kwenye mshahara wa zamani, nafikiri tutakuwa tumewaonea na itakuwa sheria kandamizi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)