Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Mwanaidi Ali Khamis (4 total)

Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Awali ya yote, napenda kutumia nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuendelea kutujaalia afya njema na uzima. Pia tuwe pole katika mzigo uliotufika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutambua michango iliyotolewa katika Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kwa Mwenyekiti wake Mheshimiwa Sillo Daniel Baran pamoja na Waheshimiwa Wabunge wote waliochangia katika mjadala huu wa hoja kwa kuzungumza na kwa maandishi hapa Bungeni. Tunawashukuru wote kwa maoni yao na ushauri wao waliotupa kwa ajili ya kuboresha Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa Miaka Mitano (2021/2022 - 2025/2026) pamoja na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2021/2022; ushauri wao tumeupokea tunawashukuru sana wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumshukuru Kiongozi wa Shughuli za Bunge hapa Bungeni Mheshimiwa Majaliwa Kassim Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kusimamia na kuwakilisha Serikali hapa Bungeni. Aidha, napenda kumshukuru Mheshimiwa Phillip Mpango Waziri wa Fedha na Mipango kwa ushirikiano na maelekezo mazuri anayoendelea kunipa katika kutimiza majukumu yangu kama Naibu Waziri wa Fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile napenda kumshukuru Mheshimiwa Mwigulu Nchemba, Waziri wa Katiba na Sheria kwa kuwasilisha hoja hii kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango na kuniongoza vyema katika kufuatilia michango iliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa, napenda niwashukuru watendaji wote wa Wizara ya Fedha wakiwemo Makatibu, Wakuu wa Idara, watumishi wote wa taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara ya Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya maneno haya ya utangulizi, napenda kuchangia hoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya kwanza, Serikali iongeze juhudi katika upatikanaji wa fedha za ziada na ugharamiaji wa miradi ya maendeleona izingatie upande wa Sekta Binafsi, kiwango kimeshuka kiasi cha trilioni nne kwa Serikali na kimeongezeka kwa trilioni 15.2. Kwa hivyo ni vyema Mpango huu wa Taifa kuendelea kutatua changamoto za upatikanaji wa fedha za ugharamiaji Mpango ili kufikia malengo na shabaha tuliyojiwekea. Ufafanuzi, Serikali itahakikisha kuwa rasilimali zote za utekelezaji wa Mpango zinapatikana kama ilivyopangwa ili kuhakikisha malengo ya utekelezaji wa Mpango yanafanikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vyanzo vya fedha vya ugharamiaji ni pamoja na Mapato ya Ndani na yasiyo ya ndani, misaada, mikopo nafuu, hati fungani na amana za Serikali; Mikopo ya kibiashara, ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi; Utekelezaji wa moja kwa moja wa taasisi na mashirika ya umma (Joint venture) na utekelezaji wa moja kwa moja wa Sekta Binafsi. Katika kuhakikisha hilo vyombo mbalimbali vya ugharamiaji mapato, vimeambatanishwa katika sehemu ya sita ya kitabu cha Mpango kulingana na eneo la ugharamiaji na aina kubwa za miradi au programu, fursa za kiuchumi, kijamii zilizopo na vihatarishi vya Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja namba mbili; Serikali ihakikishe kuwepo na upatikanaji wa taarifa endelevu za utekelezaji miradi na bajeti, dhidi ya hatua na malengo ya Mpango. Ufafanuzi, katika kuhakikisha kunakuwa na upatikanaji wa uchambuzi wa kina wa Taarifa za utekelezaji miradi, Serikali imeandaa Mifumo mbalimbali ya Kielektroniki (GEPG); Mfumo wa Msaada na Ununuzi wa Serikali (TANEBS); Mfumo wa Uhasibu Serikalini (MUSTE); Mfumo wa Uandaaji wa Usimamizi wa Bajeti (CBMCS).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupitia mifumo hii Wizara na Idara na Taasisi na Serikali zitaendelea kutoa takwimu sahihi za utekelezaji wa miradi ili kusaidia ufanyaji na tathmini za ufanisi. Aidha, Serikali imeanza maandalizi ya kuandaa mwongozo wa Kitaifa na ufuatiliaji wa tathmini za miradi mbalimbali ya maendeleo ili kuweka miongozo rasmi katika shughuli za ufuatiliaji na tathmini na kuwezesha mchakato shiriki katika ubia na uandaaji wa taratibu na usimamizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja namba tatu, Serikali ihakikishe inaelekeza Mpango Mkuu kulingana na sheria, kanuni na taratibu. Ufafanuzi, ushauri umepokelewa Serikali itaendelea kutekeleza Mipango ya Maendeleo kwa kutimiza sheria, kanuni na taratibu zilizopo katika Sheria ya Bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kutoa ufafanuzi huo, naomba kuunga mkono hoja na kukushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto
NAIBU WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI):
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa hii nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia kuniwezesha kuwepo hapa kujibu hoja ambazo zimechangiwa na Wabunge pamoja na Kamati ya Bunge. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nikushukuru wewe kwa kutuongoza pia nimshukuru Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na kuniteua kuwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto nikiwa kama mama basi sitamuangusha katika kutekeleza na kumsaidia majukumu haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimshukuru Dkt Philip Mpango kwa kuteuliwa kuwa Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuiongoza na kutuongoza katika nchi yetu. Kipekee nimshukuru Waziri wa Afya na Maendeleo ya Jamii Dkt Dorothy Gwajima kwa upendo na ushirikiano wa hali ya juu ambao amekuwa akinipa wakati wa kutekeleza majukumu yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze kamati ya kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii kwa michango yao mizuri na maoni yao waliyotupa tutajitahidi kuyazingatia katika utekelezaji wa majukumu ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nitumie fursa hii kutoa pole kwa Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Waheshimiwa Wabunge wote wananchi wa Chama cha Mapinduzi pia niwashukuru watanzania wote niwape pole watanzania wote kwa kuondokewa na viongozi mbalimbali katika nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kujibu hoja za kamati ya kudumu ya Bunge ya Maendeleo ya Jamii, kuhusu Serikali kutoa ajira kwa maafisa wa jamii na maafisa wa jamii kuwa katika vyuo vyetu vilivyoanzishwa na wataalamu hawa kutosha kuwepo wakiwa hawana ajira. Wizara imepokea ushauri wa Kamati. Aidha Wizara inaendelea kushirikiana na TAMISEMI pamoja na Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora ili kutatua changamoto za upungufu wa maafisa wa maendeleo ya jamii maafisa ustawi wa jamii katika ngazi za mamlaka za Serikali za Mitaa kadri bajeti ya Serikali itakavyoturuhusu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu maendeleo kwa vyuo vya maendeleo ya jamii kuongezwa lakini pia fedha zilizotengwa zitolewe zote kwa wakati hasa kuzingatia vyuo hivi ndivyo vinavyotegemewa kuanzisha maafisa maendeleo ya jamii ambao ndio nguzo muhimu katika maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara imetoa ushauri kwa kamati aidha, mwaka 2021/2022 Wizara imeandaa fedha kiasi cha shilingi milioni 3.6 kwa ajili ya ujenzi wa ukarabati wa maendeleo na miundombinu ikiwemo kumbi za mihadhara mabweni, maktaba na majengo ya utawala katika vyuo vya maendeleo kwa jamii ya Ruaha shilingi milioni 600, Rugemba shilingi milioni 500, Uyole shilingi bilioni moja na Mlale shilingi milioni 500 na Monduli shilingi milioni moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya kushirikiana na Wizara ya Fedha na Mipango itafanya kazi kwa utaratibu na kuhakikisha kwamba fedha hizo zilizotengwa kwa mwaka 2021/2022 zitatolewa kwa wakati ili kutekeleza kazi zilizopangwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu bajeti ya kuwezesha utekelezaji wa mipango kuzuia ukatili wa kijinsia kutengwa na kutolewa wakati badala ya kutegemea fedha za nje. Wizara imepokea ushauri wa kamati kwa mwaka 2021/2022 jumla ya shilingi milioni 791 zimetengwa kwa ajili ya kutekeleza afua mbalimbali za kutokomeza ukatili wa kijinsia. Wizara itaendelea kutenga fedha za ndani kwa ajili ya kulingana na ukomo wa bajeti.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijikite katika kujibu hoja aliyoitoa Mheshimiwa Bahati Keneth Ndimbo Mbunge wa Viti Maalum kuhusu vituo vingi vya wazee kuwa nje ya mji na vinahatarisha maisha ya wazee kutokana na kuwa mbali na vituo vya afya. Pia kuhusu huduma za afya zinazotolewa katika vituo vya wazee kupata huduma ya kwanza tu ambazo haziwasaidii wazee wanaoishi katika vituo husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inasimamia na kutoa huduma kwa wazee katika makazi 13 inayomilikiwa na asilimia kubwa ya makazi hayo yapo mjini. Mfano Fungafunga ambayo iko Morogoro Manispaa ya Morogoro, Ipuli Tabora Manispaa, Nunge Kigamboni, Njoro Moshi Manispaa, Magugu Babati Mjini, Kalandoto Shinyanga Manispaa, Makumbi, Misingwi, Mwazange Tanga Jiji, Nyambange Musoma Manispaa, Kilima Bukoba Manispaa na Kibirizi Kigoma Manispaa. Makazi yaliyo nje ya mji ni Muheza na Sukumahale Singida hata hivyo Serikali imeandaa kuisimamia huduma hizi kuhakikisha uwepo wa wahudumu wa afya katika makazi ya wazee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha kutokana na ushirikiano mkubwa uliopo kati ya wazee na halmashauri ikiwemo vituo vya afya katika maeneo ya makazi yaliyopo upatikanaji wa huduma hizo zimeimarishwa. Hata hivyo juzi mimi katika ziara yangu toka nilipochaguliwa nimetembelea Kituo cha Nunge na kuona wazee wako vizuri sana na niliwauliza wahudumu wa afya wakaniambia wanapatiwa huduma zote dawa zipo hawana wasiwasi na wanashukuru sana Mheshimiwa Rais wao Mama Samia Suluhu Hassan kwa kumteua mwanamke ambaye ataendeleza kuwalea Wazee wale kwa kushirikiana na Serikali ambayo ya Awamu ya Sita inayoendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu hoja ya Mheshimiwa Ritta Kabati Viti Maalum Watoto saba waliobakwa na mwanaume mmoja kati ya Mkoa wa Iringa Serikali iangalie sheria kulinda Watoto hawa. Napenda kumshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa ufuatiliaji wake wa karibu unaofanywa na masuala ya haki ya ustawi wa jamii ya mtoto tumeipokea taarifa na ufuatiliaji kama sehemu ya utekelezaji wa Wizara kupitia MTAKUWA.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha ili kuhakikisha haki zote zinalindwa Serikali imeongeza idadi ya mahakama za watoto kutoka mahakama tatu mwaka 2015/2016 hadi kufikia mahakama 147 mwaka 2021. Pia Serikali itaendelea kuratibu utoaji wa huduma za msaada wa kisheria kwa mashauri ya watoto mahakamani. Kupitia maafisa utawala wa ustawi wa jamii vilevile Serikali inaendelea kuimarisha dawati la jinsia la Watoto katika vituo vya Polisi ambapo hadi kufikia Aprili 21 madawati 420 yameanzishwa nchi nzima ili kuhakikisha mashauri ya Watoto yakiwemo ubakaji yanasimamiwa kwa umakini kwa lengo la kulinda haki za Watoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo tokea niteuliwe nimeamua kuandaa mikakati ambayo tutashirikiana na TAMISEMI na Mahakama na Ofisi ya Mambo ya Ndani ili kuweka mikakati hii ambayo kukomesha ukatili wa watoto katika nchi yetu, na suala hili tutapita halmashauri zote katika mikoa yote ya Tanzania kuelimisha suala hili ambapo mikakati yetu itakapokuwa sawa Waheshimiwa Wabunge nakutakeni muwe ni walezi na kutoa ushauri na hoja ambazo mtakazozitoa katika kuelimisha wananchi maana nyinyi kama mlivyoweza kuwahadaa wananchi wakakupeni kura mkafika hapa nafikiri na nyinyi ni rahisi kuwahadaa watu hawa hawa…

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Noah Lembris.

T A A R I F A

MHE. NOAH L. S. MOLLEL: Mheshimiwa Naibu Spika, Naibu Waziri ametumia lugha ambayo kidogo ina washushia Waheshimiwa Wabunge hadhi au Bunge hili kwamba tumewahadaa wananchi kuwadanganya ili waweze kutuchagua hivyo ningeomba atumie lugha ya staha au arekebishe kauli yake.

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Naibu Waziri nadhani ulikusudia kusema kuwashawishi.

NAIBU WAZIRI WA AFYA MAENDELEO YA JAMII JINSIA WAZEE NA WATOTO (MHE. MWANAIDI ALI KHAMISI):
Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante naomba nimepokea hoja nilikusudia kuwashawishi lakini katika kutekeleza na kuhamasisha wananchi imenibidi nitumie hoja ya haraka haraka kuwahadaa samahani sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wabunge wenzangu nakuombeni mikakati ambayo tutakayoipanga mtusaidie kwa wananchi kuwahamasisha ili kutokomeza ukatili katika nchi yetu na mimi nitakuwa pamoja time yoyote wakati wowote na tutatoa matangazo na namba za simu mikoa yote hadi vijijini ili likitokea suala hili niweze haraka kusimamiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nawatahadharisha ambao Wakurugenzi mahakama ma-DPP ambao wanadhorotesha kesi hizi tutakuwa sambamba, mtu ambaye tutamgundua anadhorotesha kesi hizi basi hatua za haraka tutazichukua ama kumuhamisha kumuweka mtu mwingine ili ukatili huu uondoke hapa nchini. (Makofi)

Kuhusu hoja ya Mheshimiwa Tarimba Gulam Abbas ambayo inahusu kuandaa namna bora ya kuwapatia watoto yatima walioko kwenye vituo hati za kuzaliwa ili ikiwezekana waanze shule huku ufuatiliaji wa hati zao ukiendelea. Kuhusu watoto yatima wasio na vyeti vya kuzaliwa naomba nipokee ushauri wa Mheshimiwa Mbunge. Aidha, Wizara itaendelea kuwasiliana na RITA, TAMISEMI pamoja na Wizara ya Elimu, Sanyansi na Teknolojia ili kuhakikisha kuwa watoto yatima wote kwenye vituo wanapatiwa vyeti vya kuzaliwa na kuendelezwa kielimu ili kupata haki yao ya msingi mpaka hapo watakapoanza kujitegemea wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Norah Mzeru aliongelea suala la wanawake kukumbukwa katika masuala ya afya na kuwawezesha kiuchumi ili kuweka mazingira bora kuanzia ngazi ya halmashauri. Serikali inaendelea kuwawezesha wanawake kiuchumi kupitia programu mbalimbali ikiwemo utekelezaji wa Mpango Kazi wa Taifa wa Kutokomeza Ukatili Dhidi ya Wanawake na Watoto (MTAKUWWA). Kupitia mpango huu, Serikali imewezesha wanawake kushiriki katika shughuli mbalimbali za kiuchumi kwa kuwapatia mikopo yenye masharti nafuu katika Benki ya TPB na asilimia nne ya mapato ya ndani ya Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile Serikali inaendelea kuwaunganisha wanaweke wajasiriamali na taasisi kutoa mafunzo ili kuwajengea uwezo wa kibiashara wa usindikaji wa bidhaa na matangazo ya biashara kwa njia za mitandao. Halikadhalika, Serikali inawawezesha wanawake wajasirilimali kushiriki maonesho ya kibiashara ya Sabasaba na Nanenane, program za uwezeshaji wanawake kiuchumi na makongamano ya kibiashara ili kujua mahitaji ya masoko ya bidhaa zao. Hivyo, Wizara itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kutekeleza afua na uwezeshaji wa wanawake kiuchumi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Grace Tendega, Mbunge wa Viti Maalum, anauliza Serikali imechukua hatua gani kuhakikisha wazee wanapata Bima ya Afya. Serikali kupitia Ofisi ya Rais, TAMISEMI inaendelea na zoezi la uchambuzi wa wazee ili kuwapatia vitambulisho vya matibabu. Hadi kufikia Machi 2021 jumla ya wazee wanaume 1,834,995 na wanawake 1,002,567 wametambuliwa ambapo wazee wasio na uwezo 1,042,403 wamepatiwa vitambulisho vya matibabu bila malipo. Aidha, Serikali inaendelea kukamilisha rasimu ya Muswada ya Bima ya Afya kwa wote wa mwaka 2020 ili kuwawezesha wananchi wote wakiwemo wazee kupata huduma za matibabu kwa mfumo rasmi na ulio mzuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hayo machache, naomba kuunga mkono hoja na kuwapongeza Wabunge wote waliotoa hoja zao katika kurahisisha utendaji wa Wizara yetu ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto. Nawashukuru sana kwa michango yenu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante. Kwanza nimshukuru Mwanyezi Mungu kwa kunijalia siku ya leo kuwa na hali ya uzima wa afya na kushuhudia bajeti ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum ambayo leo inasomwa tarehe 18 Mei, 2023.

Mheshimiwa Spika, naungana na Mheshimiwa Waziri kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hasan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kunipendelea na kuniamini kuwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii Jinsia Wanawake na Makundi Maalum. Lakini pia niwashukuru viongozi wote wa Wizara na watendaji kwa kutekeleza majukumu ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya pekee naomba nitumie fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Dkt. Dorothy Gwajima, Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia Wanawake na Makundi Maalum kwa maelekezo na ushirikiano wa hali ya juu anaonipa katika kutekeleza majukumu yangu katika Wizara hii.

Mheshimiwa Spika, naomba nitumie fursa hii kuwashukuru viongozi wangu wakuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lakini pia nimshukuru Mheshimiwa Dkt. Isdor Philip Mpango kwa kuendeleza vyema na kutusimamia katika Wizara yetu hii na kuhakikisha tunakwenda vyema na tunatekeleza majukumu yote ambayo tunahitaji. Lakini pia sina budi kuwashukuru familia yangu kwa kunipa wepesi na kufanya kazi zangu kwa urahisi ili kuhakikisha kazi zangu zote zinakwenda kwa salama na amani.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya naomba nitamke rasmi kwamba naunga mkono hoja kwa asilimia 100, lakini pia niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao wamechangia hoja hizi. Niishukuru Kamati ambayo imeungana na sisi katika kutuelekeza hoja zetu na kutupa maelekezo ambayo tutayafanyia kazi kadri wanavyotuelekeza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niwashukuru waunga hoja wote ambao wamechangia katika Wizara yetu hii ya Maendeleo ya Jamii, wengi wamezungumzia masuala ya ukatili wa kijinsia kwa watoto wetu. Ni kweli Serikali yetu sasa hivi tuna kazi kubwa ya kuelimisha na kutoa elimu kwa wananchi kwa ajili ya watoto wetu kutokana na mmonyoko wa maadili ambao unaendelea katika nchi yetu. Suala hili limechangiwa na Waheshimiwa Wabunge wengi, na sisi kama Wizara tutaendelea kutoa elimu kuhakikisha kwamba watoto wetu wanakuwa salama. Nitoe msisitizo kwa wazazi, wazazi, ukatili wa kijinsia unaanzia katika nyumba zetu, kwa hivyo wazazi tuhakikishe tunapata muda wa kushirikiana na watoto wetu na kukaa na watoto kuwapa elimu ili wao waweze kuelewa mila na desturi za utamaduni wetu katika nchi yetu hii ambazo zinaendelea ambapo nchi nyingi wanapenda mila zetu na desturi zetu katika nchi hii na wanapenda kuziiga; lakini wanakuja kwa mlango wa nyuma kuhakikisha kubomoa utamaduni wa nchi hii.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai tu kwa wazazi walezi jamii kujumuika katika malezi makuzi na matunzo ya ukuzi wa mtoto ili kuwawezesha famila kuwa sehemu salama kwa watoto, kuishi na kufurahia haki zao katika hatua mbalimbali. Hatua kali tutazichukua kwa wale wazazi ambao wanajua kama mtoto wao huyu ana matatizo lakini akamwachia kwa makusudi tunaomba wazazi kwamba mtoto ukimuona ana matatizo basi Wizara ipo, mfikishe pahali salama, sisi Wizara tutaweza kumhudumia.

Mheshimiwa Spika, mtoto ambaye unamuona nyumbani humuwezi sisi Wizara tuna vituo vyetu vya kulelea Watoto, tunalea watoto kwa kutumia haki zote zile ambazo wanazozihitaji. Mtoto anahitajika kupewa haki zote za msingi kuanzia elimu mavazi na kila kitu ili aweze kukua vizuri na kukua katika saikolojia nzuri, kwa sababu tunawahitaji sana. Watoto tunawahitaji kwamba, ni viongozi wetu wa kesho, tusipowapa malezi bora hivi sasa basi tutakuwa na taifa ambalo halina viongozi bora. Hivyo tujitahidini wazazi.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako Tukufu niwaombe Waheshimiwa Wabunge wanapokuwa katika majukwaa basi watoe elimu hii kwa wazazi na walezi ambao wanalea watoto hawa ili kuhakikisha malezi na makuzi yanaenda salama.

Mheshimiwa Spika, aidha, natoa wito kwa jamii na watu wenye moyo wa kutoa huduma kwa malezi na makuzi kwa watoto wa kambo kuhakikisha kwamba wanawalea watoto hawa kwa kuzingatia ubora na haki zote ambazo zinahitajika. Lakini pia kuna Waheshimiwa wengine hapa wamezungumzia kuhusu mmonyoko wa ndoa na mirathi.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna mmonyoko wa ndoa unaotokana na ukatili wa jinsia kwa wanawake. Kuna waume wengine wanakuwa hawana imani kwa wake zao. Jambo linaweza kuwa dogo lakini wao wanalichukulia kubwa na kuwapiga wengine hadi kufikia kuua. Niwaombe wazazi wenzangu wanapofikia hadi hali hiyo watoe taarifa katika vyombo husika, wasikae kimya, sheria zipo zinaowalinda.

Mheshimiwa Spika, ili uweze kuwa na haki kamilifu basi unatakiwa utoe uwazi wote mahakama itakusikiliza na ikupa haki yako. Na ndoa ambazo tunazihitaji zote zitasikilizwa. Ili mtu aweze kupata urithi basi ndoa hizo tujitahidini tunapokutana na wapendanao basi tukazisajiri ndoa zetu, ili kuhakikisha kwamba mirathi ile inakwenda kutokana na taratibu; na kila mtu anadini yake ambayo anapokea mirathi kutokana na mtiririko wa usawa na ugawaji wa mirathi hiyo.

Pia nizungumzie kuhusu watoto wa mitaani. Ni kweli kuna tatizo la watoto wa mitaani, lakini watoto hawa wanatokana na mmonyoko wa maadili kwa wazazi. Wazazi wanapokuwa hawafahamiani, wanapogombana basi hawashughulikii watoto na watoto wale wanaanza kuingia mitaani. Hili linaipa mzigo mkubwa Serikali. Serikali sasa hivi tumeamua, tumeunda Kamati ambayo itawasimamia watoto hawa ili kuhakikisha kwamba watoto ambao wapo mitaani tunawarejesha kwa wazazi wao, na mpango huo, tunamhitaji mzazi huyo tutapomkabidhi basi tutampa masharti ambayo mtoto atakaporudi tena mtaani basi tutamkamata yeye kwa sababu vipo vituo ambavyo vya kupeleka malalamiko na vipo vituo ambavyo mtoto anaweza akasaidiwa kuhakikisha anapata haki zake zote.

Mheshimiwa Spika, pia kuna vituo vyetu vya malezi ya Watoto, ambapo tuna Kikombo – Dodoma na Dar es salaam – Kurasini. Watoto hawa tunawalea na tunawapa haki zao zote za msingi na malezi bora, kwa hivyo watoto wetu hawa tuwatunze.

Mheshimiwa Spika, mmomonyoko wa maadili upo lakini tuhakikishe tunafanikisha sisi wazazi. Mtoto halelewi na mzazi mmoja au mzazi peke yake. Utamaduni wetu huko nyuma wazazi tunalelewa mpaka na majirani. Mama Salma hapa ana msemo, anasema mtoto wa mwenzio ni wako. Wahakikishe kwamba tunashirikiana, na wazazi tuwape watoto malezi bora.

Mheshimiwa Spika, pia kuna jambo jingine ambalo limesemwa hapa na Waheshimiwa kuhusu wafanyabiashara wadogowadogo. Ni kweli wafanyabiashara wadogowadogo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan amewaamini na amewajali na kuwaleta katika Wizara yetu hii ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum ili kuhakikisha na wao wanapata fursa mbalimbali za kufanya biashara ili waweze kukua kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, Wizara hii Mheshimiwa Rais ameiunda kuhakikisha kwamba amaeona kwamba wanawake wengi walikuwa wanapata tabu na biashara zao, hawana sehemu za kuzipeleka hawana sehemu za uhakikika kuhakikisha biashara zao zinafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Rais ametoa fedha takriban mikoa yote 26 na kuhakikisha kwamba kunawekwa Wizara ambazo zitawasaidia hawa wajasiliamali wadogowadogo, hasa wamachinga, nao watajisaidia katika Wizara zile na malalamiko yao yote basi katika ofisi hizo ambazo ametoa pesa Mheshimiwa Rais basi zitasaidia katika kutekeleza majukumu yao.

Mheshimiwa Spika, tumpongeze sana Mheshimiwa Rais wetu kwa kuwaona na kuwajali wananchi hawa na kuhakikisha na wao wanakua kiuchumi ili nchi yetu iwe na usawa. Kama yeye mwenyewe alivyoamua kuwa kinara wa usawa wa kijinsia basi tumshike mkono ili kuhakikisha Taifa letu linakua na linaendelea vizuri.

Mheshimiwa Spika, kuna mambo mbalimbali ambayo yamefanyika katika Wizara hii. Tunazidi kutoa elimiu Wizara yetu kuwaelimisha wananchi kuhakikisha wanapata elimu ya ukuaji wa maendeleo yao. Kwa hivyo tunawakaribisha sana katika Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii ili kupata elimu na kuhakikisha mambo yao yote yanakwenda sawa.

Mheshimiwa Spika, hoja nyingi zimesemwa hapa na wajumbe, lakini Mheshimiwa Waziri wangu ataendelea kuzijibu na hoja nyingine zitajibiwa kwa maandishi. Nikushukuru sana na niwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote ambao kwa hapa mmetoa hoja zenu na kwa ushirikiano mliotupa. Nawatakieni kila la kheri katika mafanikio ya bajeti hii ili ipite na tuendelee kushirikiana na kufanya kazi kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa nafasi hii, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum
NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya njema na kuniwezesha kusimama hapa mbele ya Bunge lako Tukufu kuchangia hoja za Wabunge ambazo wamezitoa leo tarehe 30/05/2022. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia nimshukuru Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini, kuniteuwa kuwa Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, ili kumsaidia kazi katika Wizara hii. Pia, nimshukuru Mheshimiwa Philip Isdor Mpango, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana vizuri na kutusaidia katika Wizara yetu hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kipekee nimshukuru Mheshimiwa Dorothy Gwajima, Waziri wangu ambaye ananielekeza vizuri na kunisimamia katika kuelekeza maelekezo yote katika kuendesha Wizara hii. Bila kumsahau Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mheshimiwa Kassim Majaliwa Majaliwa, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutuendeleza ili kuhakikisha kwamba Serikali yetu inakwenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niipongeze Kamati ya Kudumu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa michango yao na ushauri na maoni katika kuboresha na utendaji wa majukumu ya Wizara. Niishukuru Kamati tunajitahidi kuzingatia maoni na ushauri katika kutekeleza majukumu ya Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana wewe pamoja na Naibu wako kwa umahiri wenu wa kuliongoza Bunge hili. Pia nisikose kuwashukuru Wenyeviti ambao wanasaidia kuliongoza Bunge hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nikishukuru chama changu cha CCM kwa kunipa heshima kuwa Mbunge na hii leo nipo hapa kama Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum. Pia nishukuru UWT kuanzia ngazi ya shina hadi mkoa, mkoa hadi Taifa, bila kuwasahau akinamama wa Mkoa wa Kusini ambao wameniheshimisha leo kuwapo hapa Bungeni na Taifa likaniamini kuniwezesha kuongea hapa katika Bunge hili tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba nitamke kuwa kuunga mkono hoja hii iliyowasilishwa kwa asilimia mia moja

Mheshimiwa Spika, naomba sasa kujibu hoja za Wabunge; kwanza tumshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, mimi katika hoja hizi za Wabunge nitajikita katika sehemu nne; wamachinga, malezi na makuzi ya watoto, wazee na wafanyakazi wa ustawi wa jamii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Wizara yetu ina sera kama tano, Sera ya Maendeleo ya Jamii ya mwaka 1996, Sera ya Maendeleo ya Wanawake ya mwaka 2000, Sera ya Maendeleo ya Mtoto ya mwaka 2008 na Sera ya Taifa ya Mashirika Yasiyo ya Kiserikali ya mwaka 2001 na Sera ya Taifa ya Wazee.

Mheshimiwa Spika, tunakuja katika wamachinga; kwanza tumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuona umuhimu wa watu hawa ili kuendesha biashara zao ndogo ndogo katika Taifa hili. Napenda nimpongeze kwa upendo mkubwa aliokuwa nao katika Taifa hili, Mheshimiwa Rais ameunda Wizara hii kuhakikisha kwamba anataka kurejesha mila na desturi za Watanzania ili kuwe na utamaduni ambao tunautokea. Hivi sasa mila na desturi zote ambazo zina mmomonyoko mkubwa kwa hiyo, ameona umuhimu wa kuunda Wizara hii ili kuhakikisha kwamba yale yote ambayo tulikuwa tunapewa na wazee wetu waliotangulia basi tunayaleta na kuyafanyia kazi kuhakikisha nchi yetu hii inakuwa salama salmini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa wamachinga, Waheshimiwa wamechangia masuala mbalimbali kuwa maeneo Rafiki ili wafanye biashara zao bila kubughudhiwa.

Mheshimiwa Spika, Wizara kwa kushurikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya, Wakurugenzi na Halmashauri na viongozi wa SHIUMA tunaendelea kutenga na kuboresha miundombinu ya maeneo waliyotolewa kwa ajili ya shughuli za wamachinga. Pia tumshukuru Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kutoa shilingi milioni kumi-kumi kwa kila Mkoa kuhakikisha kazi zao zinakwenda vizuri, ili kutimiza malengo yao waliyokuwanayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hivyo, wamachinga tunao vizuri na tunaendelea kusikiliza changamoto zao kuhakikisha kwamba taratibu zote za kiofisi zinakamilika ili waweze kuwa na taasisi ambayo itakuwa mfano katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu huduma za wazee; napenda kulithibitishia Bunge lako tukufu kuwa Serikali imeheshimu na inatambua kuwa wazee ni hazina kubwa ya rasilimali katika umuhimu na ustawi wa jamii wa maendeleo ya Taifa. Aidha, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 imeweka misingi ya kibinadamu kuwaheshimu na kuwathamini wazee. Katika kuhakikisha kuwa wazee wanapata haki zao na huduma za msingi, Wizara imefanya mapitio ya Sera ya Wazee ya mwaka 2003 na kuandaa mikakati ya utekelezaji wa kuwezesha utungaji wa sheria hiyo kuhusu pensheni ya wazee, mafao kwa watumishi wastaafu kulipwa kwa mujibu wa sheria ya kuanzishwa na mfuko husika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, aidha kulingana na mgawanyo wa majukumu suala hili lilitolewa ufafanuzi na Wizara ya Fedha na Mipango kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Ajira na Vijana na Watu Wenye Ulemavu. Aidha, Serikali inatambua umuhimu wa kuanzisha mpango wa pensheni katika jamii kwa wazee wote.

Mheshimiwa Spika, pendekezo na mpango huu umeandaliwa na kuwasilishwa katika vikao vya maamuzi ambavyo vimetoa maelekezo ya masuala ya kufanyiwa kazi ili kuweka mifano mizuri na endelevu pale mipango itakapokamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu wazee na makazi yao; Wizara inaendelea kutoa huduma na matunzo ya makazi 17 ya wazee yanayowezeshwa, mfano Nunge, Kibirizi, Njoro, Kolandoto, Ngeha, Bakumbi, Ipuli, Fungafunga, Mazangwe na Nandanga na mikoa mbalimbali ambayo inapewa huduma hizi za wazee. Hadi kufikia Machi, 2019 wahudumu katika makazi hayo ni 510 ambapo wana ndugu kuwatunza katika jamii hii. Huduma zinazotolewa katika makazi hayo ni pamoja na chakula, malazi na huduma za matibabu.

Mheshimiwa Spika, vilevile wazee wanaendelea kupewa huduma mbalimbali, Serikali ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ya Awamu ya Sita inatoa fedha kila mwezi shilingi milioni 76.247 kwa ajili ya chakula. Vilevile inatoa fedha shilingi milioni 76.247 kwa ajili ya kuendeleza makazi kila mwezi. Vilevile Wizara inatoa vifaa tiba kwa ajili ya kupewa matatizo ya afya yanayowasumbua wazee hao.

Mheshimiwa Spika, wazee wanarudishwa kutoka nje ya makazi ili wasitumike vibaya. Kwa hivyo, Serikali yetu inawaenzi wazee na inawathamini kwa kila hali na mali ambazo wanahitajika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako tukufu niwaombe Waheshimiwa Wabunge wote wazee wanahitaji malezi, na sisi sote tumelelewa na wazee hawa na ndio maana leo tuko hapa na tunasimama imara kuwatetea wazee wetu hawa, kwa hivyo, wazee wanapokuwa washakuwa na hali ambayo hawajiwezi basi tuwaelimishe wananchi wetu katika majimbo yetu huko ili waweze kuwaenzi wazee wetu hawa kuhakikisha kwamba, nao wanafaidika na nchi yao, sio kuwapotezea na kuchukuliwa na Serikali. Pale tunapowachukua katika Serikali haina budi tu inabidi tuwalee wazee hawa kwa hivyo, tuwasaidieni wazee wetu, wazee ni tunu, wazee ni kila kitu katika maisha yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuhusu Maafisa wa Maendeleo ya Jamii...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muuda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Dakika moja, malizia Mheshimiwa.

NAIBU WAZIRI WA MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WANAWAKE NA MAKUNDI MAALUM: Mheshimiwa Spika, Wabunge wengi wamechangia kuhusu maafisa hawa. Naamini Serikali kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, tutahakikisha kwamba tunawaajiri na kuwapa malezi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, muda ni mdogo, michango yote mingine ataelezea Mheshimiwa Waziri kutokana na nafasi yake. Mimi nashukuru sana, niwashukuru Wabunge wote ambao wamechangia Wizara yetu hii. Ni imani yetu kwamba tutafanya kazi kwa uadilifu na michango yote ambayo mliyotupa tutaitekeleza kuhakikisha Wizara yetu hii inakuwa kama Mheshimiwa Rais alivyoitathmini.

Mheshimiwa Spika, kwa hayo yote naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, kazi iendelee. (Makofi)