Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Florent Laurent Kyombo (23 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa nafasi ya kuchangia katika Bunge lako tukufu na mimi kwa nafasi ya pekee naomba nitoe shukrani nyingi sana kwa Mwenyezi Mungu, nitoe shukrani nyingi sana kwa chama changu Chama cha Mapinduzi kikiongozwa na Mheshimiwa John Joseph Pombe Magufuli. Lakini pia niishukuru familia yangu mke wangu watoto wangu lakini kwa nafasi ya pekee pia wapiga kura wa Jimbo la Nkenge ambao walitupatia kura pacha 91% pamoja na Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, nimesoma hotuba za Mheshimiwa Rais ambazo kwa kweli zinatia faraja, zinatia matumaini zinatoa muelekeo na kuonyesha kwamba Rais yuko kwenye mstari wa kupeleka nchi yetu katika uchumi ambao ni wa juu zaidi kuliko ambavyo tumefikia sasa hivi kwa kazi nzuri iliyofanyika katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

Mheshimiwa Spika, tunaona faraja kubwa inatoka wapi katika nchi yetu, kwanza ni kusimamia tunu za Taifa; amani, mshikamano, uhuru wa nchi yetu, Muungano na Mapinduzi matukufu ya Zanzibar ndiyo inatoa fursa kwa watu walioko nje ya Tanzania kuweza kuona ni fursa nzuri ya kuweza kuwekeza katika nchi ya Tanzania na hii ni ushahidi mwingi kweli tumeona mikataba mikubwa ya madini ikirejewa tumeona mikataba ikiendelea kusainiwa mipya lakini tunaona mapinduzi makubwa ya kiuchumi na hii siyo peke yake ni kwa sababu ya Mheshimiwa Rais akiwa na wasaidizi wake mahiri kuanzia Makamu wa Rais, Mheshimiwa Waziri Mkuu pamoja na Mawaziri aliowateua.

Mheshimiwa Spika, tunaona kutokana na taarifa ya IMF ya mwaka 2019 uchumi wa nchi yetu unaendelea kupaa na Tanzania inakuwa miongoni mwa nchi kumi bora katika Bara la Afrika. Naamini kwa hotuba hii aliyowasilisha katika kipindi hiki basi tutaenda kuwa nchi ya kwanza kati ya hizo kumi katika Bara la Afrika na kuzidi nchi nyingine za Ulaya.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo na nia ya dhati ya kuona Rais anataka kutuvusha katika miaka mitano mingine ijayo niombe kuchangia kidogo katika maeneo mengine. Niseme kwamba hotuba ile imeshamaliza kila kitu, hapa tupo tunaboresha na kuweka kachumbari ili mambo yaende, lakini muelekeo wa nchi umesheheni katika hotuba ya Mheshimiwa Rais na hivyo hatuna budi sisi kama washauri, kama wasimamizi, kama watendaji kuhakikisha sasa tunayaishi haya ambayo Mheshimiwa Rais ametuambia kwenye hotuba yake ili aweze kutufikisha pale ambapo anaona inafaa kwa nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nishauri kidogo kwenye eneo la viwanda, tunaona nchi yetu ambavyo imeendelea kupambana kuhakikisha kwamba inakuwa na viwanda vya kutosha ili tuendelee kupata mchango mkubwa kutoka kwenye viwanda na tunaona viwanda vingi takribani 8,477 ambavyo vimeweza kuanzishwa katika awamu ya kwanza ya Mheshimiwa Rais. Lakini tunaona mchango wa Pato la Taifa kutoka kwenye viwanda ni zaidi ya 8.5%.

Mheshimiwa Spika, tunaona ajira zaidi ya 480,000 kutoka kwenye viwanda. Niseme kwa kaka yangu Mheshimiwa Waziri wa Viwanda tunapokuwa tunaona kiwanda chochote kinaguswa lazima tuamke tuweze kuona ni jinsi gani ya kukilinda na Wizara zetu niombe ziongee lugha moja ambayo inaweza kuinua Wizara nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nikupe mfano wa kiwanda kimoja kiko katika Jimbo langu la Nkenge, Wilaya ya Misenyi. Kiwanda hicho ni cha Oram kilikuwa ninachakata na ku-grade kahawa ukiangalia capital investment iliyowekwa kwenye kiwanda hicho, sasa hivi kimebaki ni magofu kwasababu ya mabadiliko kidogo ya kisera. Najua nchi yetu inao utaratibu mzuri wa kuhakikisha kwamba mambo yanaenda sawa, lakini mambo mengine lazima tuwe flexible kidogo kuona ni kitu gani ambacho tunaweza kufanya ili mambo yote yaweze kwenda. Kuna mabadiliko kidogo ya sheria katika kilimo kwamba kahawa zote zinunuliwe na AMCOS. Kwa hiyo, maana yake viwanda ambavyo vilikuwa vinaendeshwa vyote vika paralyse.

Mheshimiwa Spika, wananchi sasa hivi wanalia, kahawa wanazipeleka kule, zinabaki muda mrefu bila malipo kiwanda hicho kilikuwa kinatoa bei nzuri na wananchi wanalipwa kwa wakati, inachangia Pato la Taifa kinaajiri zaidi ya watu 2000 katika Wilaya ya Misenyi. Sasa hivi vijana wote wamerudi mtaani wapo wanamlilia Mbunge wao sijui nitawapeleka wapi. Kaka yangu Mwambe, kaka yangu Bashe najua nyie mko smart, naomba mkae pamoja mu- harmonize muweze kuhakikisha kwamba kiwanda hicho cha Oram kirudi kufanya kazi ili uchumi wa nchi, lakini na uchumi wa Misenyi uweze kukomboka.

Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa muda ulionipa naomba kuunga hoja hotuba ya Mheshimiwa Rais, ahsanteni. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. FLORENT G. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nafasi ya pekee nishukuru kwa nafasi ya kuchangia Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano. Nimshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuweza kutupa nguvu na sisi wote kuwa hapa kwa ajili ya kujadili Mpango huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango huu ambao umeletwa kwetu ni mpango mzuri na faraja kubwa ni kwamba, katika Mpango huo takribani asilimia 65 unatekelezwa kwa mapato ya ndani ya nchi yetu. Kuna maeneo machache ambayo mimi nataka nijielekeze kwa sababu ya huo muda wa dakika tano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza, tunaona key players ambao watahusika katika kutekeleza Mpango huu ni Halmashauri zetu za Wilaya kupitia Wakurugenzi wetu wa Wilaya, Wakurugenzi wa Majiji na Miji, lakini pia na Wakuu wao wa Idara pamoja na watumishi wote ndani ya halmashauri hizo. Ni jambo jema kwa kiongozi yeyote kuhakikisha kwamba, mazingira ya wale wote ambao watahusika katika kutekeleza Mpango huu kwa kiasi kikubwa yameboreshwa na changamoto zile ambazo wanakabiliana nazo zimetatuliwa ili waweze kutekeleza Mpango wetu vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme katika eneo hili la Wakurugenzi wa Wilaya pamoja na Wakuu wa Idara limekuwa ni eneo ambalo lina changamoto nyingi sana na hasa kutopewa mazingira mazuri kwa ajili ya kutekeleza mipango mingi ya Serikali. Badala yake unakuta katika eneo kubwa Wakurugenzi wamekuwa wakishughulishwa na shughuli nyingine ambazo hazina tija kubwa kwa Serikali na value for money haipo. Unakuta kuna tume nyingi ndogondogo zimeletwa kutoka ofisi zetu za Wakuu wa Wilaya, kutoka kwenye ofisi zetu za Makatibu Tawala wa Mikoa na kutoka kwa Wakuu wa Mikoa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyingine ukiziangalia natija yake kwa kweli unaona zinamfanya Mkurugenzi badala ya ku-focus kwenye suala la msingi na akajikita kwenye kutekeleza Mpango anashughulika kujibu hoja ambazo kimsingi nyingine unaona tija yake kwa Taifa letu haipo. Kwa hiyo, niombe sana mazingira wezeshi ya Wakurugenzi wetu wa Halmashauri za Wilaya pamoja na wasaidizi wao ambao ni Wakuu wa Idara ziweze kutolewa na waweze kutekeleza Mpango huu, ili tuweze kufikia malengo mahususi ya ndani ya miaka mitano tuwe tumefikia malengo yote ambayo yameainishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala langu la pili katika eneo hili, ni kwenye sekta ya ardhi. Mwaka 2000 Serikali ilikuja na mpango mzuri wa retention scheme ya fedha ya kodi yote ilikuwa inatolewa katika viwanja na mashamba, ikawa inakusanywa inapelekwa serikalini, lakini asilimia 20 inarudi.

Hiyo fedha ilisaidia sana katika kupanga na kupima maeneo yote kupitia Serikali zetu za Halmashauri za Wilaya, lakini mwaka 2011 Serikali kwa kuona ubora wa kazi ile iliongeza ile percentage ya retention scheme ikawa asilimia 30 na kazi zilizendelea kufanyika kwa ubora zaidi, zikapangwa na maeneo yakaainishwa, fursa za uwekezaji zikija zinakuta eneo tayari limeshapangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme mwaka 2015/2016 retention scheme hiyo ilitolewa na Wakurugenzi wa Wilaya waliendelea kuhangaika kudai zile fedha zitoke Wizara ya Fedha, hakukuwa na majibu. Mwaka 2017 yakatolewa maelekezo kwamba, retention scheme ilifutwa katika hotuba ya bajeti ya mwaka 2015/2016 kupitia Wizara ya Fedha na Mipango. Zile fedha kazi ilikuwa inafanyika kipindi hicho haikutolewa maelekezo, sasa hizo kazi zinafanyika kupitia bajeti ipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka leo Halmashauri za Wilaya kupitia Idara ya Ardhi, zimebaki zimekatwa miguu, kazi hizo hazifanyiki kwa ufanisi. Tunatambua kazi nzuri ambayo Wizara ya ardhi imefanya kwa kutatua migogoro, lakini kwenye suala la kupima na kupanga na kudai fedha ambazo zinatakiwa ni masuuli ya Serikali yake, imebaki ni giza. Tuwaombe kwa muktadha huo hiyo retention scheme irudi na irudi katika asilimia 40 ili hizo kazi zifanyike kwa kuzingatia dira ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru. Naunga mkono Mpango ni mzuri kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, ahsante niungane na wasemaji waliotangulia kuunga mkono hoja iliyoko mbele yetu, lakini pia kuipongeza sana Serikali kwa Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Miaka Mitano, ambao unaonekana ni taswira njema kwa ajili ya kuhakikisha kwamba nchi yetu inapiga hatua kimaendeleo.

Mheshimiwa Spika, nilitaka nijielekeze moja kwa moja kwa juhudi za Serikali ambazo kupitia mwongozo ulioletwa mwaka 2018, ambao ulikuwa ni mkakati madhubuti wa Serikali kuziwezesha Mamlaka za Serikali za Mitaa kuweza kutelekeza miradi ya kuchochea upatikanaji wa fedha ili ziweze kujitegemea na hivyo kutoa huduma sahihi kwa wananchi. Fedha hizo za kuwezesha miradi ya kimkakati ziliendelea kutolea na Serikali kutoka Serikali Kuu; na tumeona katika sehemu kubwa zimekuwa za tija na zimeleta matokeo chanya.

Mheshimiwa Spika, niseme katika maeneo ambayo miradi ya kimkakati imeweza kutekelezwa kwa ufasaha tumeona matunda mazuri, moja wapo ni ushahidi kupitia taarifa ya CAG. Jiji la Dar es Salaam kabla halijavunjwa kwa zile hesabu zilizofungwa tarehe 30 Juni mwaka jana lilikuwa na uwezo wa kujitegemea kwa asilimia 484; kwa hiyo maana yake lilikusanya Bilioni 16 na lina uwezo wa kutumia Bilioni tatu. Kwa hiyo tunaona kama tuna miradi mingine ya kimkakati, huduma za wananchi kama kujenga zahanati, kujenga vituo vya afya na Mengine kuchangia barabara kupitia TARURA jiji hilo lilikuwa na uwezo. Lakini siri ya mafanikio ilikuwa ni nini, ni uwezeshaji uliotoka Serikali Kuu, ni mbegu iliyopandwa katika baadhi ya Mamlaka za Serikali za Mitaa moja wapo ikiwa hilo Jiji la Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, tunaona sasa hivi mkakati wa Serikali unavyokwenda na katika bajeti hii inayokuja ni ushuhuda tosha, Ofisi ya Rais TAMISEMI imeelekeza Mamlaka za Serikali zote 185 kutenga bajeti kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya, kila Mamlaka ya Serikali za Mitaa kituo kimoja. Najua kupitia huu uwekezaji uliokwenda kule kupitia miradi ya kimkakati vituo hivyo vitajengwa; na baadhi ya halmashauri ambazo hazijapata uwezeshaji huo inawezekana zikatekelezwa kwa kusuasua, lakini niseme ni mwanzo mzuri. Kwa hiyo tunachotakiwa kufanya ni nini? kwa kuishauri Serikali. Ni kukuhakikishia sasa huu mkakati ambao uliundwa madhubuti ambao umeanza kuonyesha matokeo chanya uendelezwe.

Mheshimiwa Spika, mkakati huu kwa sasa haufanyi kazi ulisimamishwa na Serikali, na maelezo hayakuwa wazi kuonyesha kwamba umesimamishwa kwasababu gani na unaanza lini?

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niombe kwa kusema kwamba Serikali, kwa kazi nzuri ambayo tumeshaiona matokeo yake ni kwanini tusiwezeshe? Tukiziwezesha halmashauri hizi maana yake tunategemea sisi tunakuwa tunatoa maelekezo kwamba sasa mwaka huu kama nchi yetu kuna kigezo fulani cha kuanzisha miradi fulani weka katika bajeti zenu mradi moja, mbili, tatu unaweza kutekelezwa kwa ufasaha na tutaona maendeleo makubwa sana. Katika mwongozo huo kuna baadhi ya vitu ambavyo inatakiwa kama Serikali kuvifanyia kazi. Suala la kwanza vipo vigezo madhubuti 14 katika mwongozo huo, baadhi ni vizuri baadhi vinahitaji kufanyiwa marekebisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano suala moja wapo ni kuwa na hati safi. Tunaona kwenye taarifa ya CAG leo zipo halmashauri jumla 63 hazina hati safi, anayeadhibiwa ni nani? Ni yule ambaye alisababisha, kama mtaalam wetu au mwananchi? Kwa nini tunapeleka adhabu kubwa kwa mwananchi; ambapo Serikali ingeweza kupeleka fedha za kuwezesha miradi ambao utasaidia baade apate huduma tukamuadhibu kwasababu hana hati safi? Mwananchi hajui hati safi, haijui kabisa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niiombe sana Serikali, sisi wote ni waumini wa kuhakikisha fedha zinasimamiwa vizuri, kwa umadhubuti kabisa, lakini sasa suala hilo naomba tuliangalie kwa mapana, kama kuna hati ambayo sio safi wale wawajibishwe lakini fedha ziendelee kupelekwa kwenye halmashauri.

Mheshimiwa Spika, wakati naendelea kumalizia dakika zangu zilizobaki kupitia meza yako hiyo nimuombe Waziri wa Fedha na Mipango. Zipo barua nyingi ambazo zimepelekwa kwake kwa zile halmashauri ambao zimeshakidhi vigezo. Moja wapo ni Wilaya ya Misenyi Jimbo la Nkenge ambapo ilipelekwa barua tarehe 4/09/2019 ya mradi wa maghala nane katika mpaka wa Mutukura kukiwa na stendi ndogo pamoja na jengo la biashara.

Mheshimiwa Spika, niombe, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, wakati unakuja kwenye bajeti angalau uweze kuhakikisha kwamba mradi huo ndani ya Wilaya ya Misenyi unaweza kutekelezwa. Tupo mpakani mwa Uganda mradi huo utaleta matunda ndani ya muda mfupi.

Mheshimiwa Spika, barua hiyo haina mradi wa Wilaya ya Misenyi peke yake, iko miradi mingine. Babati TC nao waliomba Bilioni 5.1 kujenga Stendi, kuna Meru DC nao waliomba Bilioni 10 kuna Lindi MC waliomba ujenzi wa Stendi 7.8 pamoja na Soko katika Manispaa yetu ya Lindi. Kwa hiyo niombe…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: basi nikushukuru naunga mkojo hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi na mimi niungane na wachangiaji waliotangulia kuipongeza Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa kwa kazi nzuri wanayoifanya ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nishukuru kwamba Jeshi la Ulinzi limekuwa likifanya kazi kubwa na hasa katika Wilaya na Majimbo ambayo yapo mipakani mwa Nchi yetu kama Mheshimiwa Waziri alivyosema katika hotuba yake na Wilaya ya Misenyi ni mojawapo ya sehemu ambayo Wizara ya Ulinzi imefanya kazi kubwa kuhakikisha amani na usalama ndani ya Wilaya yetu ya Misenyi inakuwepo na hasa katika eneo la kudhibiti wahamiaji ambao walikuwa wanatoka nchi za jirani kuja kufanya machungo ya mifugo yao ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi nzuri hiyo katika eneo hilo, tunaomba maboresho kidogo katika Jeshi letu la Ulinzi. Ukiangalia katika eneo ambalo lipo mpakani kabisa eneo la Kata ya Kakunyu, vijiji vya Kakunyu, Bugango na Bugwenkoma; mpaka wa Jeshi letu upo karibu kilometa 20 kutoka mpakani, maana yake unaacha vile vijiji nyuma na nchi ya Uganda halafu wenyewe mpaka upo mbele ya vijiji. Kwa kweli pamoja na kazi nzuri ya Jeshi letu wananchi wamekuwa wakipata taabu sana kwasababu kweli lazima Jeshi letu lijiridhishe unapokuwa unatoka eneo hilo kuja Makao Makuu ya Wilaya, kwa hiyo katika msafara huo unakuta na baadhi ya wananchi wanapata kero ndogo ndogo ambazo zinaweza kudhibitiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana, kwa kuwa Mheshimiwa Waziri unajua kabisa Wilaya ya Misenyi ilitenga maeneo mazuri kule kwenye mpaka kabisa zipo heka za kutosha. Mimi ningeshauri Wizara yako ione sasa ule mpaka ambao upo katikati baada ya vijiji uweze kuhamia katikati ya nchi ya Uganda na Tanzania ili wananchi wetu sasa vijiji hivyo nilivyotaja wawe huru kuendelea na shughuli zao na pale wanapokuwa wanakwenda Wilayani basi wasipate bughudha nyingine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma Randama ya Wizara ya Ulinzi, tunaona kazi nzuri wanayoifanya na hasa katika eneo la ushirikiano na mamlaka za kiraia. Kuna kazi nzuri zimefanyika, lakini katika eneo hilo, kuna suala lingine ambalo ningeweza kushauri Wizara iboreshe. Ni mahusiano au utatuzi wa migogoro kati ya jeshi letu ulinzi na wananchi. Wilaya ya Misenyi wote tunajua kwamba ulikuwa ni uwanja wa vita vya Kagera ambavyo vilihitimishwa mwezi Juni, 1979. Kwa hiyo, umeacha maafa mengi sana katika eneo hilo na wananchi wanapokuwa wanaendelea mambo hayo kuyaona wanahisi bado tupo ndani ya vita.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1978 Jeshi letu lilikuja na wananchi walikuwa tayari kujitoa kwa ajili ya kutoa rasilimali kuwezesha jeshi letu ili kupigana vile vita ambavyo kimsingi sisi wananchi tulikuwa na maslahi nayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Kata ya Kyaka, Kijiji cha Kurifani, Kitongoji cha Biawamara wananchi walitoa maeneo yao kwa ajili ya kuhakikisha jeshi letu linakaa salama, linaweka nyenzo zake, zinapigana vita vizuri. Na wananchi walitoa eneo ambalo lenyewe lilikuwa liko wazi na wao wakabaki na mashamba yao na miji yao maisha yakaendelea. Jeshi likatulia pale likafanya kazi nzuri iliyotukuka na tukafanikiwa kumkimbiza Nduli Iddi Amini nje ya mipaka ya Tanzania, lakini pia na kuwakomboa Waganda. Baada ya miaka baadaye sasa Jeshi limebadilika likawa mwenyeji wale wanachi wamekuwa wahamiaji. Maana yake sasa hivi wananchi ndio wanavamia eneo la jeshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, inasikitisha kidogo, katika eneo hilo eneo ni kubwa mno na eneo ni pori kubwa mno, wananchi wana mashamba yao na miji yao, lakini hata hiyo miji hawaruhusiwi kuendeleza, huruhusiwi kulima, huruhusiwi kufanya chochote, kwamba ni eneo la jeshi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nikuombe kupitia kiti chako, Serikali ya Wilaya imeandika sana kupeleka suala hili Wizara ya Ulinzi kwa Katibu Mkuu, lakini kitu chochote ambacho kimefanyika mpaka leo. Mimi mwenyewe nimekuja hapa Bungeni nimemuandikia Mheshimiwa Waziri ki-note kwamba kule Misenyi, Kyaka, Kyawamara kuna matatizo haya nafikiri kwa sababu ya majukumu yako naomba ulifanyie kazi na nikuombe Mheshimiwa Waziri twende kule ukaone hali mwenyewe kwa sababu hii ni hali ambao inatatulika ukienda mwenyewe pamoja na wasaidizi wako tuweze kuwaokoa wananchi, kutowagombanisha na jeshi letu ambalo linafanya kazi kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Katika suala lingine Wilaya ya Misenyi, kuna eneo ambalo tulikuwa wahanga ambapo mabomu ya Iddi Amini kweli yalikuwa pale na yakabomoa eneo la kanisa, kwa sasa hivi yaliyobaki ni magofu. Tunaishukuru Serikali tukufu ambayo imeweza kujenga Kanisa na wananchi waliendelea na ibada zao katika eneo lingine. Eneo hilo liko kati kati ya Kata ya Kyaka ambayo ni mjini kabisa ambapo sasa kwa sababu lipo katika eneo la mwinuko inaonekana katika kata nzima ambayo ni mjini pale. Sasa mahema hayo yamebakizwa ni magofu ambayo ni vipande vya kuta vya hilo kanisa ambalo lilikuwepo enzi hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wakiangalia yale mabaki wanahisi kama vita vinarudi au hatuna mahusiano mazuri na nchi ya Uganda au kuna nini ambacho Serikali isingeweza kutengeneza eneo hilo likawa ni zuri, likawa la kivutio la kumbukumbu nzuri badala yake limekuwa ni magugu yamejaa pale na mwananchi akikosea kidogo akapita katika eneo hilo, hivyo viboko atakavyoambulia siyo vya nchi hii.

Kwa hiyo, mimi niombe sana na niishauri Serikali eneo hilo linaweza kufanyiwa matumizi mawili either Jeshi likawekeza sehemu nzuri ya kuweza watu kupumzika pale. Ni view nzuri ya Mto Kagera ambayo kila mmoja anauona Mto Kagera kwa kona zake na Daraja la Mto Kagera. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kama Jeshi haliwezi, linaweza likatoa eneo hilo kwa Serikali ya Wilaya kwa Halmashauri ikawekeza kitu kizuri na wananchi au ikawa ni eneo la open space wananchi wakawa wanapumzika pale. (Makofi)

Kwa hiyo niombe sana jeshi letu liweze kuangalia masuala haya kwa mapana na hiyo ni sambamba na uwanja wa mashujaa ambao Mwalimu Nyerere alipokea wanajeshi wetu kutoka Uganda baada ya vita. Na eneo hili lipo kati kati ya nji, ni pori, ni nyasi ndefu na hivyo unakuta inaleta taswira mbaya pale maana yake inaonekana ni eneo la jeshi lisilofanyiwa usafi, ni eneo la jeshi lisiloendelezwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niomb jeshi letu pamoja na kuwa na haki yakutunza maeneo yake ya kumbukumbu na kihistoria kwa sababu mahali pale sio sehemu ya vifaa vya kijeshi, kwa mfano; uwanja huo wa mashujaa umeshazungukwa na Halmashauri, umezungukwa na wananchi, unawezekana ukawekezwa katika taswira nzuri, ukaendelea kumilikiwa na jeshi, lakini ukatumia kwa shughuli za Kiserikali kama ambavyo wanatumika. Ni eneo ambalo viongozi wetu wa Kitaifa wakija pale tunafanyia mikutano. Tukiwa na makongamo tunafanyia mikutano pale, lakini kwa kweli ukiuona uwanja huo ni uwanja ambao haupo nadhifu na kwa kweli ukisema kwamba majeshi yetu yalikuja yakapokelewa na Mheshimiwa Amiri Jeshi Mkuu wakati huo inakuwa haileti tija nzuri kwa taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo niombe sana, mheshimiwa Waziri pamoja na Wasaidizi wake baada ya kipindi hiki cha Bajeti twende Wilaya ya Misenyi wakakague sehemu ya Byawamara, maeneo ambayo yanaleta changamoto kwa wananchi, wakaangalie lile eneo la kanisa ambalo limebaki kama kumbukumbu, wakaangalie uwanja wa mashujaa ndani ya Wilaya ya Misenyi, uweze kuwekewa mkakati madhubuti viboreshwe na viweze kuwa ni kumbukumbu njema kwa ajili ya Taifa letu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee kuwashukuru Jeshi wanaendelea kufanya kazi, sisi ambao tupo mipakani tunaona mchango mkubwa wanaoufanya na niendelee kumshukuru pia na Mkuu wetu wa Wilaya lakini kimsingi ni tunda la Jeshi ambaye ni Kanali Dennis Mwila ambaye amekuwa ni nguzo kubwa katika eneo letu kuhakikisha ulinzi wa Wilaya ya Misenyi unakuwepo. (Makofi)

Kwa hiyo, nipende pia kusema kwamba baadhi ya maeneo kama wachangiaji wengine walivyosema tunahitaji kuwa viongozi ambao wamepitia katika vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha kwamba maeneo hayo yanaweza kulindwa vizuri na amani wananchi hao inaendelea kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naomba nikushukuru kwa nafasi naunga mkono hoja. Niombe basi Mheshimiwa Waziri baada ya majukumu hayo akaitembelee Wilaya ya Misenyi tuweze kutatua hizo changamoto za wananchi. Nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu ya Fedha. Niungane na Wabunge wenzangu kuipongeza Wizara hii chini ya uongozi wa comrade Mwigulu Nchemba, Waziri wa Fedha, lakini pia na ndugu yangu Mheshimiwa Masauni, Katibu Mkuu pamoja na viongozi mbalimbali wa Wizara hiyo ikiwa ni pamoja viongozi wa taasisi ndani ya Wizara ya Fedha.

Mheshimiwa Spika, mimi nitajikita katika Fungu 45 ambayo ni Ofisi ya Taifa ya Ukaguzi chini ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ambapo Ofisi hiyo imepewa majukumu kupitia Ibara ya 143 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Jukumu kubwa la Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali ni kuhakikisha kwamba inafanya ukaguzi wa mapato na matumizi kama yalivyoidhinishwa na Bunge lakini pia kutoa taarifa Bungeni na hapo Bunge lako Tukufu linapata fursa ya kuweza kuitafsiri na kuishauri na kuisimamia Serikali yetu. Hayo yote yamekuwa yakifanyika kwa weledi mkubwa kupitia Ofisi ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini kwa nafasi ya pekee niendelee kuipongeza Serikali, nilikuwa napitia bajeti mbalimbali katika miaka iliyopita katika Ofisi ya CAG ambapo tumeona mwaka 2019/2020 Ofisi yetu iliweza kupewa bajeti yake kwa asilimia 109 ya ile bajeti ilikuwa imejiwekea. Hivyo tukiona ufanisi wa kazi wa Ofisi ya CAG kama inavyofanya tunajua ni kwamba Serikali imeweka mkono wake kuhakikisha kwamba Ofisi hiyo inafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Spika, lakini mwaka 2020/2021 bajeti ya CAG iliongezeka kidogo na tunaona mpaka tarehe 30 Aprili, Ofisi hiyo iliweza kupewa fedha na Serikali kwa asilimia 92. Naamini katika miezi michache iliyobaki hiyo bajeti yake itaweza kukamilika kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hili tunaona CAG anafanya kazi kwa kushirikiana na Bunge lako Tukufu kupitia Kamati za Kudumu ambazo zinafanya kazi na Ofisi ya CAG. Hivyo tuendelee kuipongeza Wizara ya Fedha kupitia Ofisi ya CAG kwa ushiriki mzuri pamoja na hizi Kamati ambazo zinafanya kazi pamoja na Ofisi hiyo za PAC, LAAC pamoja na Kamati ya Bajeti na Kamati zingine za kisekta kadri ambavyo wanakuwa wanaona ushirika unatakiwa. Kwa hiyo, tumeendelea pia kuimarishwa katika uweledi ili tuweze kutafsiri taarifa za CAG vizuri na kuweza kuleta mchango mzuri katika Bunge lako Tukufu ili Bunge lako sasa liweze kuishauri na kuisimamia Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, nikiangalia kwa undani Ofisi ya CAG, mtaji mkubwa ambao inauhitaji kuupata ni kupitia wataalam wake, hasa Wakaguzi wetu kuwa na weledi zaidi katika kufanya nao kazi. Hiyo inatokana na kujihuisha kutokana na taratibu zingine za Kimataifa ambazo sisi kama Tanzania ni waumini wa taratibu hizo. Tunao mfumo wa IFRS
- International Financial Reporting System ambao ndio tunaufuata, lakini tuna IPSAS ambao ni International Public Sector Accounting System ambao tunaufuata. Wataalam wetu hawa wakiwezeshwa vizuri, kila muda wakawa wanahuishwa vizuri katika mafunzo ya Kitaifa na Kimataifa, tunaamini tutapata taarifa ambazo ni nzuri, ambazo zimeenda kwa kina na kuweza kuishauri Serikali vizuri pamoja na kuisimamia.

Mheshimiwa Spika, nikiangalia katika bajeti ya Fungu 45 katika suala la kuweza kuwa-equip Wakaguzi wetu waweze kusimama vizuri kwa kusimamia sheria zetu za nchi yetu, lakini pia na standards za Kimataifa, sioni kama tuna nia ya dhati ya kuweza kuwafanya Wakaguzi wetu, pamoja na ueledi walionao leo, pamoja na uzoefu wa kazi walionao, kuendelea kupata elimu zaidi na kuendelea na standards za Kimataifa ambazo zinabadilika baada ya muda mfupi mfupi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nikiangalia katika bajeti hii, naona katika sehemu zote nimepitia katika Idara mbalimbali za Ofisi ya CAG, hakuna sehemu ambapo unaona wataalam wetu wanaenda kupata mafunzo hasa ya nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna maeneo madogo ambayo yameonesha kwamba, kuna mafunzo ya nje kupitia Idara ya Utawala, lakini ni fedha kidogo sana. Pia kuna huduma za kiufundi katika ukaguzi, zimewekwa fedha kidogo sana. Kwa hiyo, ukiangalia mabadiliko ya nchi yanavyokua, tunahitaji kuhakikisha kwamba, wataalam wetu au Wakaguzi wetu katika Ofisi ya CAG wanaendelea kupewa mafunzo ambayo yatawafanya wafanye kazi kwa weledi na hivyo kuweza kuleta taarifa ambazo ni nzuri katika Bunge lako Tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikiangalia pia, CAG hawezi kufanya kazi peke yake anafanya kazi na Bunge lako Tukufu. Utaungana na mimi Bunge hili jipya la Kumi na Mbili lina asilimia 67 ya Wabunge wapya. Na asilimia hiyo 67 ndio Wabunge wameenda kwenye kamati ambazo zinafanya kazi na CAG. Kwa hiyo, nilikuwa nauona kama mwaka wa fedha 2021/2022 ni mwaka ambao Serikali ingejikita kuongeza bajeti kule kwa CAG kuweza kuwa-equip Wakaguzi wetu, lakini kuweza kuwapa mafunzo vizuri Wajumbe wa Kamati ambazo zinafanya kazi na CAG, ili sasa baadaye tuendelee kupata matunda mazuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia katika maeneo hayo, hakuna kinachoonyesha kwamba, kuna nia ya dhati kuhakikisha kwamba, Wakaguzi wetu pamoja na Wabunge ambao wanahitaji kukaa na kutafsiri taarifa za CAG ili ziweze kutusaidia katika kufuatilia miradi ya maendeleo, katika kuangalia hesabu za Serikali, haipo. Kwa hiyo, pia mama yetu Rais wetu mpendwa, mama Samia Suluhu Hassan, amemwelekeza CAG aendelee kupanua wigo wa kuweza kufanya ukaguzi. Hata hivyo, ukiangalia bajeti aliyopewa mwaka, 2021/2022 haionyeshi nia hiyo ya dhati. Mwaka jana alipewa bajeti ya bilioni 80, lakini mwaka huu imeongezwa ni bilioni 80.9. Sasa hata maelekezo ya Mkuu wa Nchi hatuyaoni yaki-reflect katika bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe kitu cha kwanza, Ofisi ya CAG iongezewe fedha, lakini ofisi hii iendelee kuongezewa fedha kwa ajili ya wataalam wetu kuendelea kujifunza mafunzo ya ndani lakini pia na mafunzo ya nje. Kama ni suala la hali ya kidunia ya corona, tunashukuru Serikali yetu ya Awamu ya Tano, iliweza kutupa mafunzo mazuri na Serikali yetu Awamu ya Sita inaendeleza. Maana yake tunatakiwa kuendelea kuishi na huo ugonjwa na ndio maana hata Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, ameunda Tume nzuri ya Kudhibiti Corona imekuja na maoni, wale ambao wanaenda kufanya kazi watachanjwa na kazi ziendelee. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hakuna kizuizi ambazo kitafanya Wakaguzi wetu washindwe kwenda kupata mafunzo kwa ajili ya kuweza kutoa ushauri mzuri. Hakuna mafunzo ambayo yatazuiliwa kwa Waheshimiwa Wabunge wa Kamati zinazohusika, washindwe kwenda kupata mafunzo kwa sababu, ya kisingizio cha Corona. Corona tutaishi nayo na ni sehemu ya maisha yetu.

Mheshimiwa Spika, nikiangalia katika majukumu makubwa ya Ofisi ya CAG imejiwekea jukumu ambalo ni la msingi ambao ni kutoa mafunzo kwa Kamati zote ambazo inafanya nazo kazi ambazo ni Kamati ambazo ziko chini ya ofisi yako. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika mafunzo hayo ni kufundisha Kamati hizo pia, kwa ajili ya kufuatilia miradi ya maendeleo. Kwa hiyo, katika eneo hilo likiweza kuboreshwa vizuri, basi tunaamini kazi ya CAG itaweza kufanyika kwa weledi na wanaokuwakilisha katika Kamati kwa niaba yako ili kuleta maoni yao hapa, basi watakuwa wanafanya kazi kwa weledi na tunaamini sasa nchi yetu itasonga mbele kwa kuwa inasimamia fedha ambazo zinaidhinishwa, inasimamia fedha ambazo zinakusanywa na inasimamia fedha ambazo zinatumika katika taasisi zetu mbalimbali, katika halmashauri zetu, mashirika pamoja na taasisi nyingine za Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, niendelee kwa kusema kwamba, nikiangalia katika maeneo mengine, fedha iliyokuwa imetengwa ya mafunzo katika kipindi kilichopita, sasa hivi hata mafunzo ya ndani kwa CAG imepungua. Kwa hiyo, maana yake hatuoni nia ya dhati ya wataalam wetu ndani ya Ofisi ya CAG kuweza kupata mafunzo hayo.

Mheshimiwa Spika, vilevile nikiangalia katika kitengo cha uratibu wa shughuli za Bunge ambacho kinatuhusu sisi katika kupata mafunzo, nimeona katika kasma 22010 imewekwa bajeti kidogo ya mafunzo ya ndani ya Kamati zako, lakini hakuna kasma yoyote ambayo inahitaji Wabunge waende ku-share mawazo na usimamizi kama Kamati hizo nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niendelee kusisitiza suala hili ni la msingi na naliongelea kwa nia ya dhati sio kwa sababu, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya PAC, lakini ni kwa sababu ya nia ya dhati kwamba, Wakaguzi wetu wapate mafunzo, Kamati zinazohusika zipate mafunzo ili tuweze sasa kuishauri Serikali vizuri na malengo mahususi ya nchi yetu yaweze kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi kwa ajili ya kuchangia Taarifa za Kamati hizi tatu ambazo zimewasilishwa katika Bunge lako tukufu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwanza kabisa naunga mkono hoja katika taarifa zote zilizowasilishwa na Kamati za PAC, LAAC na PIC. Pia nipongeze Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan ambaye yeye ametoa mazingira rafiki kuweza sisi wote kukaa hapa katika Bunge lako Tukufu na kuweza kujadili taarifa za Kamati hii kwa ajili ya Serikali yetu.

Mheshimiwa Spika, nitakuwa mchovu wa fadhila nisipoipongeza Ofisi ya CAG ambayo kwa weledi na uzalendo imeleta taarifa zilizoshiba na sisi tukaweza kuzipitia na kudadavua na kuweza kutoa maoni kwa ajili ya maslahi ya Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, niseme kwamba taarifa ya CAG tumeipitia, tumeiona, tumehoji Wenyeviti wa Taasisi na Maafisa Masuuli pamoja na wasaidizi wao. Katika maeneo hayo nitaomba nijikite katika eneo moja, dosari katika usimamizi wa mikataba na athari zake katika matumizi ya fedha za umma.

Mheshimiwa Spika, tutaona katika maeneo haya michango mingi imejikita katika eneo hili. Ni kwa sababu gani? Kwa sababu eneo hili ni eneo ambalo linagusa maslahi ya wananchi moja kwa moja, ambapo Mheshimiwa Rais anatafuta fedha ili ziende kuleta thamani ya fedha katika miradi mbalimbali ya maendeleo lakini tunaona watu wachache, wanaweza kufanya utendaji wa uzembe, usiozingatia misingi ya kanuni na sheria na kuweza kutumia hizi fedha kinyume cha taratibu.

Mheshimiwa Spika, naomba nijikite katika mfano wa baadhi ya taasisi ambazo tunaona katika utendaji kazi wake zimeweza kwenda ndivyo sivyo. Nianze na Taasisi ya TANROADS. TANROADS ni taasisi ambayo imepewa dhamana ya kujenga miundombinu ambayo inagusa moja kwa moja maslahi ya mwananchi katika miundombinu ya barabara na maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, TANROADS wapo wataalam, wapo wanasheria wazuri, wapo viongozi ambao wamepewa dhamana na Serikali na ukiangalia wanajua sheria zote, lakini tunaona kwamba katika eneo hili badala ya kuzingatia sheria na kanuni zinazoongoza taasisi hiyo, watu wanatoa certificate za kumaliza kazi, siku zinaisha za kisheria 28, Mataifa ya nje 56 bado fedha hazijalipwa, Serikali inaingia katika hasara. Tunaona hasara ya bilioni 68.7.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nakokotoa kwa ufupi kuona hizi fedha kwa bajeti yetu ya TARURA ile ambayo majimbo yetu tunapokea bilioni 2.5, majimbo 30 yote yangepata bajeti ya mwaka mzima, lakini hizi fedha zote zimehama kwenda kulipa riba kwa sababu ya kuchelewesha malipo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo hili haliwezi kuvumilika. Kwa hiyo kupitia Bunge lako tukufu niombe hawa watumishi ambao walitakiwa kufanya kazi kwa weledi wajitathmini na Bunge lako litakuja na mapendekezo ambapo niombe Wabunge waniunge mkono ili iweze kuingia kama moja ya maazimio ya Bunge lako tukufu.

Mheshimiwa Spika, eneo la pili ni eneo la Mkataba wa Mradi wa REA I, REA II, REA III ambao kwa uchache tu CAG ame-spot Mkoa wa Mara. Kwenye scenario hii unaona kampuni moja tu inaweza kutumia milioni 329 za Serikali haiguswi, haisemwi chochote, haichukuliwi hatua. Ukiangalia mambo mengine kwa kweli yanaumiza. Hii kampuni ya Derm Electrics Tanzania Limited hizi pesa ilinunua vifaa vya kuweza kusimamisha miundombinu ya umeme. Miundombinu haikusimamishwa, watu zaidi ya 4000 hawakupata huduma. Hivyo vifaa badala ya kuvikabidhi TANESCO, imebaki navyo na mpaka leo hakuna hatua yoyote ya kisheria ambayo imechukuliwa. Sasa unajiuliza katika eneo hili hivi kiburi hiki hii kampuni inakitoa wapi?

Mheshimiwa Spika, watumishi ambao wanasimamia kampuni hii na miradi hii kiburi cha kutokuchukua hatua wanakitoa wapi? Niombe kupitia Bunge lako Tukufu. Tabia hii tukiiacha ikaendelea itaambukiza na watumishi wengine ambao ni wazalendo kwa nchi hii waweze kuiga matendo ambayo siyo mazuri. Kwa hiyo niombe sana katika Bunge lako Tukufu tuweze kuchukua hatua ambazo baadaye nitapendekeza.

Mheshimiwa Spika, wakati roho yangu inaendelea kuuma na kusononeka kwa hujuma hizi dhidi ya Serikali, nikapitia hotuba ya mbeba maono wa nchi hii Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan alivyohutubia Bunge lako Tukufu tarehe 22 April 2021. Naomba kunukuu. Katika eneo hili tukiangalia hotuba ya Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan ukurasa wa 32 amesema yafuatayo; “Serikali ya Awamu ya Sita kama ilivyokuwa Awamu ya Tano itaendeleza jitihada za kuimarisha nidhamu ya uwajibikaji kwenye Utumishi wa Umma. Tunakusudia kuimarisha taasisi na pia kuweka mifumo ya uwajibikaji ambayo itahakikisha kwamba viongozi na watumishi wa umma katika ngazi zote wanawekewa malengo yanayopimika. Mfumo uliopo wa sasa ikiwemo mikataba kati ya kiongozi na walio chini yake pamoja na OPRAS tutaiangalia upya.”

Mheshimiwa Spika, nitakuja kueleza kitu juu ya OPRAS. Hata hivyo, Mheshimiwa Rais akaenda mbali akasema: “Tutawapima viongozi na watumishi kwa namna wanavyotimiza majukumu yao na msisitizo akasema hatutawaonea aibu viongozi na watumishi wazembe, wezi, wabadhirifu wa mali za umma.”

Mheshimiwa Spika, leo Mheshimiwa Rais ameshatuwekea mambo kibla, tumsogezee kwenye 18 amalize kufunga mabao. Hawa wote ambao wamehusika katika kuhujumu fedha za Serikali, tumsogezee amalize kazi. Mheshimiwa Rais ahangaike kutafuta fedha, lakini usimamizi huu kupitia Bunge lako Tukufu, tuweze kumsaidia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo lingine, tunaona kwamba katika mapendekezo ambayo ningeomba kuleta kwenu, niombe kweli kupitia Bunge hili, Bunge liridhie watumishi wote waliosababisha hasara hizi na Maafisa Masuuli wote wachukuliwe hatua za kinidhamu na kisheria pia mamlaka za uteuzi zinapoona yule aliyekosa na anahusika, ni suala dogo la Mheshimiwa Rais na viongozi waandamizi kuchukua hatua mara moja ili tutoe huu uozo uliopo ili tuweze kuleta watu wengine ambao wanaweza kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la pili ambalo niombe Bunge lako Tukufu, kupitia hotuba hii ya Mheshimiwa Rais kuna kipengele ambacho nimesoma anasema OPRAS tutaiangalia upya. OPRAS ni tathmini ya utendaji kazi ya watumishi wote wa umma, kuanzia Ma-CEO na wasaidizi wao. Ningeomba maboresho yanayoletwa yawahusu Maafisa Masuhuli. Katika eneo hili nimeangalia vipengele nane vilivyopo katika OPRAS vyote hakuna kitu kinachoongelea suala la hoja za Serikali za CAG katika taasisi husika. Kwa hiyo unampima kiongozi wa taasisi, hii OPRAS ambayo ni kipimo cha kazi, lakini hakuna sehemu ambapo tunamuuliza kwa nini ulipata hoja hii? Kwa nini hukujibu hoja hii na kwa nini uliweza kupata hati isiyoridhisha? Hakuna.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo kupitia Bunge lako Tukufu niombe katika vipengele nane hivi kiongezwe kipengele cha tisa ambacho kitasaidia kuweka kipengele cha hoja za CAG ili Mkuu wa Taasisi awe anatathminiwa na anayemtathmini akienda pale inabidi agote kidogo ili kuhakikisha kwamba yote ameya-capture.

Mheshimiwa Spika, katika pendekezo la mwisho na ombi kwa Bunge lako Tukufu, nikuombe, kwanza kabla ya ombi hili nikupongeze kwa kuwa wewe umekuwa mtu wa maono na kabla ya taarifa hii kuja ulituongezea muda wa kufanya kazi kwa hizi Kamati zote tatu, tangu tarehe 10 sisi tuko hapa, tunakaa mpaka usiku. Pamoja na muda na maono yako ya mwanzo tumeweza kupitia taarifa hizi chini ya asilimia 10.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo ninachokuomba, kwa uweledi wako na maono, uangalie namna njema ambapo Kamati hizi zitaongezewa muda ili tuweze kupitia taarifa hizi kwa kina na kwa wingi. Hakika nakwambia kwa hili utakalolifanya kwa Taifa hili, tuko tayari kukujengea mnara mmoja ubandikwe Dodoma na mwingine tuupeleke Dar es Salaam kwa sababu utakuwa umefanya kazi ya kizalendo ambayo haijawahi kutokea katika nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sana haya mambo ni mema kwa ajili ya nchi yetu, tuungane pamoja kumsaidia Mheshimiwa Rais ili hizi fedha zisimamiwe vizuri, miradi ionekane kwa wananchi katika majimbo yetu yote na baada ya hapo Serikali itapongezwa.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru kwa nafasi na naomba kuunga mkono hoja taarifa zote ambazo zimewasilishwa. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu. Na mimi niungane na wenzangu ili kuipongeza Serikali kwa nzuri inayofanyika, na hasa mimi nitajikita katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ukurasa wa 13 na 51 ambao unaongelea suala la afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru sana kwamba Serikali imeendelea kuboresha miundombinu kwa kufanya ukarabati, lakini pia kujenga miundombinu mipya ya afya, na hasa tumeona Hospitali za Rufaa za Kanda, za Mikao, Halmashauri Vituo vya Afya na Zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kupongeza tena Serikali tumeona fedha zilizotokana na mkopo wa 1.3 trillion, bilioni 466 zote zilielekezwa Wizara ya Afya ili zikanunue dawa na Vifaa Tiba na wananchi wetu waendelee kupata matibabu ambayo ni bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hili kwenye fedha hizo zinazopelekwa Wizara ya Afya asilimia 60 na 70 ni fedha ambazo zinanunua dawa, na dawa hizo zinatakiwa zisambazwe katika vituo vyote vya kutolea huduma dhamana hiyo imepewa MSD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nitajikita katika utendaji kazi wa Shirika letu la MSD; na ninaomba kabla sijaongelea sana MSD niwape chimbuko kidogo la MSD.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiangalia Sera ya Afya ya Juni mwaka 2007, naomba kunukuu, kwamba; “Dawa na vifaatiba ni bidhaa muhimu katika kutoa huduma za afya zilizo bora, bidhaa hizo zinahitajika utaalam na umakini mkubwa wakati wa kuagiza, kutunza na kusambaza”.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nasimama mbele yako nikisitika sana, Shirika letu la MSD halina mtaalam hata mmoja wa kusimamia haya ambayo yameainishwa katika Sera ya Afya. Ukiangalia katika watumishi 700 walioko ndani ya MSD ni asilimia 6 tu ya wataalam wa dawa walioko pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia katika kanda zetu 10 zote ambazo MSD inasimamia kusambaza dawa kule hakuna mtaalam wa dawa. Serikali imesomesha wataalam wa dawa kwa gharama kubwa sana, na nikisema katika rank ya gharama ya kusomesha wataalam tunaanza na doctor of medicine tunaenda na doctor of medicine and surgeon tunaingia pharmacist, ni taaluma ambazo zinasomeshwa miaka mitano na internship mwaka mmoja. Pharmacy inasomwa miaka minne na internship mwaka mmoja, ni gharama kubwa kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunao professor pharmacist’s wako 13, leo tunao PhD holders pharmacist wako 20, leo tunao Masters holders 167 ambapo kati ya hao wamesomeshwa procument na supply chain management system; lakini masikitiko yangu ni kwamba ukienda pale MSD leo idara ambayo ni mahususi kwa ajili ya kufanya makadirio ya dawa Tanzania inaongozwa na mtu wa manunuzi tu sifa kubwa ni mwanajeshi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba Serikali mniambie hivi dawa zimegeuka kuwa bunduki au risasi? Ni kitu gani ambacho kinafanya wataalam waachwe pembeni halafu waende kuchukua mtu wa kawaida? Inasikitisha sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na leo tunatarajia matokeo makubwa kutoka MSD, haiwezi kutokea; sisi wote kwa imani zetu kila mmoja anaomba afike peponi, pale Mwenyezi Mungu atakapomchukuwa, lakini lazima ufe kwanza. Leo tukitaka MSD ifanikiwe lazima tuhakikishe tunabadilisha tunarudi kwenye Sera ya Afya ambayo ilisema inahitaji mtalaam na umakini mkubwa, wataalam wakabidhiwe ile taasisi iweze kuendeshwa. Tofauti na hapo tutakuja kuona billions of money zinapelekwa MSD zinazama leo nikisimama hapa nikirudi miaka 3 nyuma MSD dawa zilizo-expier ni bilioni 26 kwa sababu gani hakuna mtaalam.

Mheshimiwa Mwenyekiti,

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuambie mimi bahati nzuri ni mfamasia dawa zinatengenezwa katika ma-group nikikuambia group la fetharisporincy kuna dawa kama 100 leo ukiniletea dawa ya cephalexin na cephoxine zote ni fetharisporincy lakini kama sina moja kwenye stoo nitakuambia hii cephalexin itakufaa, lakini wenzetu kwa sababu hakuna wataalam akiambiwa dawa A kama haipo ni out of stock, wanarudi nyumbani kule dawa iliyopo nyingine ina-expire. Leo tunapoteza bilioni 26 ambayo ni sawa na zahanati tunazopeleka milioni 50 522.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini vituo vya afya vya milioni 500 ni vituo 52 hapa tunaangalia miaka mitatu miaka mitano hadi 10 ijayo ni nini; Mheshimiwa Rais ameliona hili. Wakati anapokea taarifa ya CAG alisema MSD inatakiwa ifanyiwe overall, ifanye maboresho makubwa, na tumsaidie kumshauri kwamba kilichotokea na kinachosababisha MSD isifanikiwe ni kwa sababu wameacha utalaam wamepeleka watu wa interest ambazo hazijulikani ninaomba Serikali kabidhi taasisi hizi za wataala ili wataalam hawa waweze kufanya kazi ya kitaalam na matokeo makubwa yaweze kuonekana lakini kila siku wananchi wataendelea kuachana dawa hazipo na dawa zina-expire…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kushukuru kwa kulinda muda.

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, leo taasisi ambazo zinafanya vizuri kwa sababu ya kusimamiwa na watalaam wake…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MWENYEKITI: Haya Mheshimiwa Tabasamu!

T A A R I F A

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, hawezi kusema ni mtu wa kawaida yule mwanajeshi aliyeko pale ni Daktari Bingwa na aombe radhi namuomba Mheshimiwa Mbunge aombe radhi katika jambo hilo hansard iwe sawa (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kyombo unaipokea taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, namheshimu sana kaka yangu Tabasam taaluma ninayoiongelea naongelea pharmacists. Nikienda kwenye mifumo ya ufamasia nikakuambia pharmacokinetics ya dawa nitakuambia…

MHE. TABASAM H. MWAGAO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: …nitakuambia procurement and management supply chain kwakweli naheshimu taaluma nyingine zote. Na nilikua naenda huko kuhitimisha. Kwa hiyo mimi ninaposema vile nasema mtu ambaye ame-specialize kwenye dawa, si kwenye matibabu daktari ana…

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: …ndicho kitu ninachoamaanisha. Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi naomba tuishauri vizuri Serikali, tusilete ushabiki, ili twende vizuri Mheshimiwa Rais wetu ili naye aweze kupumzika kutafuta fedha nyingine kwa ajili ya miradi…

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: … kwamba pale tusiweke watu ambao wanaweza wakakaa na dawa, wakasimamia dawa, wakambaza dawa na zikafika kwa wananchi.

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nikupe mifano mizuri ya taasisi ambazo zinasimamiwa ambazo zinasimamiwa na taaluma za pharmancy ambazo…

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: … zimefanya vizuri tunayo TMDA, mamlaka ya chakula…

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, Spika kaniamba...

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mamlaka ya dawa na vifaatiba inafanya vizuri ndani ya nchi na nje ya nchi

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, na inatoa gawio hata kwa Serikali.

MWENYEKITI: Taarifa Mheshimiwa Masaburi!

T A A R I F A

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Mheshimiwa Mbunge anayeongea kwanza afute ile kauli ya kusema yule si mtaalam, ni mtu wa manunuzi. (Makofi)

MWENYEKITI: Hiyo taarifa au nikufuta kauli?

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, afute kanuni ili...

MWENYEKITI: Kanuni namba ngapi?

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti ili hansard zikae vizuri…

MWENYEKITI: Unasimama kanuni namba ngapi Mheshimiwa Mbunge?

MHE. JULIANA D. MASABURI: Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni taarifa.

MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Kyombo, endelea. (Makofi)

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru, tukisikiliza vizuri hoja yangu nimesema mtaalam wa dawa, na nchi hii hakuna mtaalam wa dawa, sijasema medical doctor, nimesema mtaalam wa dawa. Naomba tujikite kwenye hoja ili kusaidia nchi hii ili wananchi wetu wawe wanapata dawa na shughuli zote ziweze kwenda kwa mujibu wa taratibu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,

MBUGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa

MWENYEKITI: Taarifa wapi ahh Mheshimwa wa Ulinzi

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante!

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba ulinde muda wangu.

T A A R I F A

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa. Taarifa nyingi zimetolewa lakini na mimi nilitaka kuongeza sauti kwamba hatuwezi kusema Mwanajeshi ni mtu wa kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili imeshaelezwa kwamba yeye pamoja na kwamba ni Mwanajeshi ni professional yake pia ni udaktari, tatu Chief Executive Officer wa taasisi yeyote si lazima awe na taaluma ya fani hiyo, anaweza kufanya kazi akiwa na taaluma nyingine yoyote ilimradi ana wataalam wa kufanya naye kazi kwa hiyo naomba ieleweke kwamba si sahihi kabisa… (Makofi)

MWENYEKITI: Taarifa ya Waziri wa Ulinzi, ni taarifa.

WAZIRI WA ULINZI NA JESHI LA KUJENGA TAIFA: Mheshimiwa Mwenyekiti, jenerali kwamba ni mtu wa kawaida. Ahsante.

MWENYEKITI: Unapokea taarifa amesimama kwa kupitia kifungu namba 77 taarifa.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sijui ambapo sieleweki ni wapi namheshimu sana Waziri wangu mpendwa lakini suala nililosema….

MWENYEKITI: Unapokea taarifa au haupokei?

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipokea.

MWENYEKITI: Ahsante, endelea

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninachomaanisha nasema ni mtaalam wa dawa na sijapinga kuwepo kwa brigedia pale, nimesema asilimia sita tu ya wataalam walioko MSD ndio wataalam wa dawa, lakini asilimia iliyobaki yote ni watu wasaidizi ni wanasheria ni wahasibu, nikasema katika kanda 10 hakuna mtaalam wa dawa kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huo ndio mchango wangu. Kwa hiyo naishauri Serikali iweze kuboresha taasisi yetu ya MSD ifanya vizuri iwatumie wataalam iliyowasomesha kwa bei kubwa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru, naunga mkono hoja ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Afya
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia katika Wizara hii ambayo inagusa Maisha yetu. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Rais Dct. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri anayoifanya katika kuiimarisha Wizara hii. Pia tunaona kazi nzuri ambayo inafanyika katika ujenzi wa hospitali za rufaa za mikoa ambazo ziko chini ya Wizara, na kazi kwa kweli imeboreshwa baada ya kuwa chini ya Wizara.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimpongeze Mheshimiwa Waziri, dada yangu Mheshimiwa Ummy, kazi unaifanya nzuri pamoja na Naibu Waziri wako Mheshimiwa Dkt. Mollel, mnajitahidi sana, nafikiri pongezi nyingi mmezipata kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge. Hatupongezi kwa ajili ya kufurahisha; kazi ukiwa unafanya tunakuambia na kama mambo hayaendi vizuri pia tuna kushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, najua viongozi hawa hawafanikishi bila kuwa na wasaidizi wao wa chini; Katibu Mkuu Kaka yetu Seif, Naibu Katibu Mkuu Grace Maghembe (Dkt.). Pia Mganga Mkuu wa Serikali Prof. Tumaini Nagu na madaktari wote, naona jopo limekamilika. Nikiangalia Wakurugenzi wako hapa, naona akina Dkt. Subi, akina Dkt. Chandika, wapo wote, Prof. Lugajo, wote wapo. Kwa hiyo unayo timu nzuri ambayo inaweza kuleta mageuzi makubwa katika Wizara yako, na wengine ambao sikuwataja lakini nawaona hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nitajikita katika maeneo kama manne, na eneo la kwanza nataka kushauri kwenye suala la NHIF. Tunajua Serikali ilichukua jukumu la kuboresha au kuona ni jinsi gani ya kusimamaia Mfuko wa NHIF, na ikaondoa form 2C. Form 2C ni fomu ambayo mgonjwa akikosa dawa katika kituo alichoenda kuandikiwa basi anapata fursa ya kuipata sehemu nyingine kwa utaratibu ambao Serikali iliuweka.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni jambo jema kwa Serikali, lakini mimi wasiwasi wangu, na sintofahamu yangu ni kuangalia maandalizi gani mazuri yaliyofanyika ili kitu hiki kisiathiri mfumo wa matibabu; na madaktari wapo hapa, niliowataja na ambao sikuwataja, wanajua basic practice ya medicine.

Mheshimiwa Naibu Spika, anapoenda mgonjwa kwa daktari akaandikiwa dawa inatakiwa apate dawa ile ile. Unless daktari abadilishe ile dawa, lakini akilenga zaidi katika matumizi ya dawa hii kumsaidia mgonjwa, asilenge katika upatikanaji wa dawa iliyoko stoo ili apewe mgonjwa; suala ambalo leo ndio linalofanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwa kweli hilo suala linaniuma kama mtaalamu wa dawa ilhali nikijua wanaosimamia sera hii na upande huu ni madaktari ambao ni wabobezi, na ni wazuri, wanajua umuhimu wa mgonjwa kuandikiwa dawa fulani akaipata dawa hiyo ambayo daktari mwenyewe amemuandikia inamsaidia kiasi gani.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatuishii kwenye form 2C, kupata ukakosa dawa stahiki, tunaenda na wale ambao ni watoa huduma wa kusaidia pale Serikali inapokuwa haijafikisha mkono wake. Pharmacy za watu binafsi ambazo zinatoa huduma hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, Tumeenda mbali, ikaonekana kwamba zile pharmacy ambazo ziko nje ya hospitali, kwamba zinauza dawa za wizi hazitakiwi kuwepo. Mheshimiwa Waziri mimi nakupenda sana, najua unachapa kazi, lakini mpaka leo hizo pharmacy hazina vibali; tulizinyima vibali. Sasa sijajua intention ni nini; kwamba tunataka zi-phase out au tunataka kuzifuta. Lakini ni kosa gani limefanywa na hizo pharmacy?

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi nirejee tena, madaktari hawa tunaowaona sura, mimi nimesomea Muhimbili na hawa wote ni colleagues, tunajua jinsi ambavyo wamefaidi zile pharmacy zilizoko pale nje kupata dawa nje na ile ambayo inatakiwa labada kutoka nchi kama vile Ujerumani na Egypt. Yote hii inasaidia Serikali, pale ambapo inakuwa haijafikisha huduma Serikali yetu inaendelea kuonekana kwamba inafanya kazi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na hayo, niseme katika eneo hilo…

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

TAARIFA

NAIBU WAZIRI WA AFYA: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimpongeze mwenzangu, anachangia vizuri sana na input yake ni muhimu sana na ina hoja. Lakini natataka tu nimpe taarifa kwamba, kwenye hilo eneo la form 2C, kwenye fedha ambazo zimeokolewa na Bima ya Afya, bilioni 115, asilimia 80 zinatokana na form 2C. kuna watumishi ambao wamekamatwa wako mahakamani sasa hivi, na kuna maduka ya dawa ambayo sasa hivi yamefungiwa, yamenyang’anywa bima na wengine wako mahakamani yanatokana na form 2C. Kwa hiyo form 2C ndicho kichochoro chenyewe. Jana tu, wiki mbili zilizopita tulikuwa pale kutokana na form 2C, tuliokoa milioni 600, ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Ahsante sana, Mheshimiwa.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naipokea taarifa, maana hapa tunajenga, wala hatubomoi. Serikali pale ambapo inaweza kusimamia vizuri rasilimali za Serikali isimamie vizuri. Mimi nilitaka kushauri, kama kweli inaonekana kuna pharmacy ambayo imeshiriki kuiba dawa za Serikali, penal code zipo. Ukienda section 302 unaweza kumpeleka na ukamfunga zaidi ya miaka saba. Ambacho hatujakiona, ambacho Serikali imetuonesha ni kwamba kuna mtua ambaye ameshapelekwa mahakamani amefungwa kwa sababu amekutwa na dawa za Serikali.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa haya kama hayaonekani hatuwezi kusema kwamba hayafanyiki. Lakini kama Serikali inachukua hatua sisi tunawapongeza sana, hakuna ambaye ana kipingamizi na hatua mnazozichukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini mimi niachosema ni kuhusu maandalizi mazuri ya mazingira. Leo mgonjwa akienda, watu wanatibiwa hapa, kwenye hospitali yetu nzuri kwa Dkt. Chandika, lakini ukienda pale dawa ukakosa unaishia kuambiwa bwana tafuta utaratibu unaowezekana. Sasa, ni suala ambalo mimi nafikiri ushauri muuchukue Dkt. Mollel yaani usiendeleze taarifa ili tuweze kuboresha kuona sasa ni namna gani ambayo tunaweza kuboresha eneo hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala la bei, nafikiri Mheshimiwa Waziri wewe ni shahidi, nimekuletea vipimo ambavyo kipimo hicho kwa cash ni shilingi laki mbili lakini ukienda kwa Bima ni milioni moja. Vipo kwa evidence na kwa kuonesha wazi. Tukasema tuboreshe katika maeneo hayo. Fedha zinapotea kwa Bima ya Afya lakini na sisi wenyewe tumeweka bei ambazo si za soko. Kwa hiyo haya yote yakiboreshwa mimi nafikiri tunaweza kukaa vizuri na Serikali yetu ikaendelea kutoa huduma kwa wananchi kama tulivyoahidi kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili niongee suala la MSD. Mimi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais, alichukua hatua kuiboresha chini ya Wizara ambayo ni Mheshimiwa Waziri na Mheshimiwa Naibu Waziri wanaendelea kusimamia. Lakini kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri amesema Menejimenti bado; Menejimenti ndiyo inasaidia; hata kama Mtendaji Mkuu yupo, hata kama bodi ipo, iweze kufanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi naomba nishauri, Mheshimiwa Waziri pale ambapo tumechelewa kidogo basi kimbiza hiyo Menejimenti ikamilike. Lakini na Wakurugenzi wako wote wa MSD wote wanakaimu. Sasa unapokaimu maana yake maamuzi ya kufanya pale huwezi kuyafanya kwa kujiamini. Hata kama mtu anataka kumshauri Mkurugenzi Mkuu wa MSD atakuwa anasita kwa sababu hajui kwamba kiti alichokikalia ni cha kwake.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia pamoja na suala ambalo limejadiliwa na Waheshimiwa Wabunge wengi. Kwamba waongezewe MSD mtaji. Tunachotaka kuona ni ni kwamba dawa zinafika kwenye zahanati na vituo vya afya pamoja na hospitali, ili sasa MSD ionekane kwamba inafanya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine niishauri Wizara kuhusiana na masuala ya majukumu makubwa ya Wizara, ambayo ni Kinga na Tiba. Suala la Wizara pamoja na kututibu lakini lazima kinga iwe ni bora zaidi. Katika eneo hilo kuna suala ambalo Mheshimiwa Waziri analijua. Tuna suala la kemikali ambazo zinatumika katika jamii kwa mfumo wa vipodozi, kuna zinazotumika kwa mfumo wa chakula; lakini zimeachwa zinaendelea kuzagaa katika soko letu, na mwisho wa siku anayeathirika ni Mtanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, na mimi juzi nilikuwa naangalia taarifa ya Habari ya RPC Mwanza, watu saba wamekula chakula ugali na furu, wawili wakafariki saba wako hoi; lakini dalili anasema wametapika. Hizo zote ni dalili ambazo kwa daktari anajua kwa hiyo ni mycotoxin, ni sumu kuvu. Sasa, sumu kuvu unapoiacha ikadhibitiwa na watu ambao hawana taaluma ya udaktari sioni kama tunaisaidia nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo mimi bado nimuombe Mheshimiwa Waziri mimi, nay eye ni mwanzilishi wa hili suala; bidhaa hizo mbili za chakula na vipodozi sisemi ziende wapi wala wapi lakini zirudi katika Wizara yake inaweza ikawa kinga kwa wananchi ili waweze kuzi-manage vizuri. Lakini anapoacha bidhaa huria vipodozi, dada zangu mtanisamehe, kuna vitu vingine ambavyo tunatumia kama wataalamu lazima tuseme ukweli, kwamba kesho na kesho kutwa tunapata Kansa ya Ngozi, tunaanza kuwa na magonjwa ambayo ni hormonal imbalance kwa sababu ya kutumia vitu ambavyo havitakiwi. Sasa ni nani ambaye anaweza kusimamia hili suala likaenda vizuri ni Waziri wa Afya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niombe Wizara ijitahidi katika eneo hilo, na najua Mheshimiwa Waziri analifahamu basi aendelee kushauri kule kukubwa ili aweze kusikilizwa mpaka hili liweze kufanyika. Baada ya kusema hayo kuna la mwisho, Mheshimiwa Waziri umekuja Mkoa wa Kagera umetutembelea umeona jinsi tulivyo changanyikana na Uganda na…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Kyombo.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, niombe basi na sisi Mkoa wa Kagera tuweze kupata hospitali ya rufaa ya mkoa yenye hadhi ya mkoa ule ili tunapokuwa jirani na Uganda, Rundi na Rwanda tuweze kuwa na…

NAIBU SPIKA: Ahsante, muda wako umekwisha.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi. Niungane na wasemaji waliotangulia kumpongeza Mheshimiwa Ummy Mwalimu, lakini pia Mheshimiwa Silinde na Mheshimiwa Dkt. Dugange kwa kuendelea kuaminiwa na Mheshimiwa Rais na niwapongeze pia kwa kumpata Katibu Mkuu mzuri Profesa Shemdoe.

Mheshimiwa Spika, nataka nijielekeze katika maeneo machache ya kushauri ndani ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI na hasa yenyewe ikiwa ni kiungo kikubwa katika kuwafikia wananchi maana yake kutekeleza sera na miradi mbalimbali kwa wananchi wetu. Nianze na utayari wa kazi na ari ya kazi ndani ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa kama Taifa. Mojawapo ya sifa ya kiongozi mwema ni kuweza kutambua upungufu au mahitaji halisi ya watendaji kazi wake ambao wanategemea waweze kutekeleza sera na miradi mahsusi mbalimbali ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, sifa nyingine ya pili ni kuweza kuwapa motivation, maana yake kuwaamini na kuwatambua. Nimekuwa nikiongelea hili suala mara kwa mara na leo limepata wizara yenyewe inayohusika. Eneo la halmashauri nikimaanisha Wakurugenzi wa Serikali za Mitaa na Wakuu wa Idara, nisikitike kusema kwamba imekuwa ni kama punching box ya viongozi wa aina mbalimbali, viongozi wa ngazi mbalimbali kuwa kundi hili la watendaji ambao tunawategemea kufanya kazi za Serikali.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia mazingira wanayofanyia kazi hawastahili kuhukumiwa kama wanavyohukumiwa. Mheshimiwa Ummy Mwalimu amefanya kazi ya Uwaziri katika Wizara mbalimbali kwote alikotoka ameacha alama na watu wanamkumbuka, nimwombe sana katika michango tunayoitoa hapa aipokee, aitafakari na akaifanyie kazi kule. Wale watu wanafanya kazi usiku na mchana, watu hawalali wanatekeleza miradi. Haya anayoyasikia tunayasema humu mengine ni kweli yana ukweli wake, lakini wachache hawawezi kufanya wote waonekane kwamba hawafai. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana baada ya kipindi chake cha bajeti atenge muda wake, bahati nzuri amepata viongozi wazuri Profesa Shemdoe ni tunda la U-DED, Dugange huyu amekuwa DMO na amekuwa RMO, anajua mazingira mazima kwenye halmashauri. Mheshimiwa Silinde anajua, akaa nao aangalie mapungufu waliyonayo, akiwa-console matokeo makubwa ndani ya TAMISEMI atayaona, lakini tukikaa kuwanyooshea kidole, kila anayesimama Mkurugenzi, Mkurugenzi wengine hatujajifunza taratibu za uendeshaji wa halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naongea haya nilikuwa Mkurugenzi na nimetoka hapa naingia hapa Bungeni, lakini mazingira yaliyopo kule kama tungekuwa tunapima job weight inawezekana Wakurugenzi wangekuwa kati ya watu wanaofanya kazi nyingi ndani ya Taifa hili, kuliko watu wengine, lakini ni kwa sababu ni kundi ambalo halisemewi, kila mtu anawageuza wale ni punching box, hivyo niombe auchukue ushauri wangu aufanyie kazi. Wale wachache ambao ni kweli wameshindikana, tutawachukulia wameshindikana, lakini wale learned brothers and sisters wanafanya kazi kwa weledi, naomba wawatumie wafanye kazi tutekeleze miradi kule chini.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu wa pili, ni upande wa afya. Naomba niipongeze TAMISEMI kwa kazi nzuri ambayo wamefanya hasa katika eneo la afya. Tunaona tumejenga hospitali nyingi katika kipindi hiki, tumejenga vituo vya afya, tumejenga zahanati. Haya mambo yamewezekana kwa sababu ya usimamizi mzuri wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo niombe tu tuendelee na speed kubwa ya kuweza kuboresha. Katika eneo hili naomba nishauri, nimesoma randama ya Fungu 56, kuna fedha ambazo Serikali wanazipata kutoka kwa wafadhili za Mfuko wa Pamoja wa Afya (Health Sector Basket Fund).

Mheshimiwa Spika, mwaka jana fedha hizi kutoka kwa wafadhili zilichelewa fourteen point something billion, tukafunga mwaka tunazo, lakini mpaka leo hizo hela bado hazijaingia kwenye mfumo kwenda kufanya kazi kule. Fedha hizi ni za muhimu sana kuweza kuongeza nguvu kwa fedha zinazotokana na Serikali kwa ajili ya kununua dawa, kununua vifaa tiba, chanjo lakini na supervision kule chini, lakini mpaka mwezi Februari kwa ripoti ya TAMISEMI hizi fedha fourteen point one billion bado hazijaenda.

Mheshimiwa Spika, suala hili sio la TAMISEMI kwa sababu sisi tunashauri Serikali na Serikali ni moja tuiombe Wizara ya Fedha masuala haya ya kutopata vibali vya matumizi ya fedha yamekuwa ni mengi. Serikali yetu yenyewe inaweza ikawekea checks and balance yenyewe kwamba fedha zikija nje ya muda kuna jinsi ambavyo wanaweza wakaingia kwenye bajeti wakazipa vibali. Haya tumeyaona sio kwa TAMISEMI peke yake hata kwenye fedha za barabara tumeona hapa zilikuwa zimechelewa sana, wakandarasi, Wizara ya Ujenzi wakawa wamesimama kazi. Kwa hiyo naomba kushauri kwamba hizi fedha ni za msingi najua TAMISEMI inawezekana wanakimbizana kuomba vibali ili waweze kuhakikisha kwamba zinaingia katika mfumo na zinafanya kazi.

Mheshimiwa Spika, ushauri wa tatu ni kwenye force account. Nchi hii imepiga hatua ndani ya miaka mitano kwa utaratibu mzuri wa force account ambao tumeutumia katika miradi mbalimbali, lakini tumepata michango mingi kutoka kwa Waheshimiwa wengine. Eneo hili lina mapungufu kidogo na hasa upungufu kidogo na hasa kama walivyosema ni kwa upande wa wataalam.

Mheshimiwa Spika, tumeanzisha TARURA ma-engineer wote tumewachukua tumewapeleka TARURA, kwa kweli mimi niombe hatuhitaji kuwa na majengo ambayo lifespan yake itakuwa ni chini ya miaka mitano baada ya miaka mitano unakuta jengo linapasuka, lote linaharibika. Niwaombe sana TAMISEMI Waheshimiwa Wabunge wengine wametangulia kulisema, tujitahidi tupate Wahandisi wawe stationed moja kwa moja kwa Wakurugenzi, wale wanaoazimwa TARURA ikitokea kazi ya TARURA wanaacha ile kazi ambayo ni ya msingi ipo pale. Najua eneo hili kwa force account tutaendelea kusonga mbele, tuombe basi tuongezewe watalaam.

Mheshimiwa Spika, suala lingine nishauri kwenye suala la TARURA. Najua kuna formula ambayo wanaitumia TARURA kuweza kupata fedha ndani ya wilaya fulani, lakini kuna vigezo vingine nahisi hatuvipi kipaumbele. Ukiangalia Mkoa wa Kagera ni Mkoa ambao kwanza una mvua nyingi katika kipindi kizima cha mwaka, karibu asilimia 75, lakini sehemu hiyo imejaa mito, imejaa maziwa kila sehemu kuna maji na water table ipo juu sana. Sasa tukipewa bajeti sawa na eneo lingine ambalo kimsingi lina hali conducive kwa barabara hatuwezi kulingana, hizo barabara ndani ya muda mfupi zinaharibika.

Kwa hiyo niombe sana kupitia Ofisi yetu ya Rais, TAMISEMI wauangalie kwa jicho la pekee Mkoa wa Kagera na specifically Wilaya ya Misenyi. Tunao mtandao wa barabara kilometa 921, tunapopata milioni 700, hata ile formula ambayo wanapiga kilometa moja kwa milioni mbili haitoshi. Kwa hiyo niombe sana…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, baada ya mchango huo, nakushukuru kwa nafasi na naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi na mimi kuchangia katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nafasi ya pekee naomba nitumie fursa hii kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri na hasa katika ujenzi wa barabara na miundombinu ndani ya Jimbo la Nkenge, Wilaya ya Misenyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pongezi hizi zinakwenda sambamba na salamu za Wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, nikitoa pongezi kubwa kwa Mheshimiwa Waziri, Prof. Mbarawa, kwa kazi nzuri pia na Naibu Mawaziri wako Ndugu yangu, Mheshimiwa Eng. Kasekenya na Mheshimiwa Atupele Mwakibete kwa kazi nzuri mnayoifanya katika eneo la ujenzi na uchukuzi. Pia niwapongeze Makatibu Wakuu wote wawili wa sekta zote mbili na Naibu Makatibu Wakuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, niwapongeze watendaji wenu ambao wako ndani ya Mkoa wa Kagera wakiongozwa na Engineer Yudas Msangi, Meneja wetu wa Mkoa wa Kagera pamoja na wasaidizi wake ndani ya ofisi hiyo, wanafanya kazi nzuri kwa yale malengo na kazi mnazowapangia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mambo mawili makuu ambayo nitaongelea, nitashukuru lakini pia nitaomba. Suala la shukrani la kwanza, nishukuru Mheshimiwa Rais kupitia Wizara hii kwa kutujengea daraja zuri na kubwa la Kitengule, na Mheshimiwa Waziri umekuja pale, lile daraja limekamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na daraja hilo Mheshimiwa Waziri ukatuahidi barabara ya kilometa 25 ya kutoka Kibaoni – Bunazi kwenda mpaka Kitengule. Ninakushukuru sana kwa sababu uliahidi na manunuzi yameshafanyika na mkandarasi sasa hivi anafanya mobilization kwa ajili ya kuanza kazi. Kwa hiyo, ni faraja njema, nikufikishie salamu za upendo, na shukrani zimuendee pia Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru pia kwa kutekeleza ahadi za viongozi. Katika Serikali ya Awamu ya Tano, Mheshimiwa Rais aliahidi barabara ya Mutukula kwenda Minziro. Hii barabara ilikuwa inapita katikati ya msitu. Na Mheshimiwa Waziri mkamtuma Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Kasekenya akaja pale akaona hali halisi. Leo tunavyoongea mmeshafumua ule msitu na barabara inaendelea kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, ambacho ninaomba katika eneo hilo, speed ya utengenezaji wa barabara hiyo siyo nzuri. Mategemeo mazuri ya wananchi wa Mutukula na Minziro kurahisisha usafirishaji katika eneo hilo basi niombe kwa kazi nzuri mliyoianza iweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nishukuru kwa ujumla barabara zote zinazosimamiwa na TANROADS, nikiangalia barabara ya Katoma kwenda Bukwali, ipo katika kiwango kizuri. Barabara ya Amshenyi kwenda mpaka Ruzinga iko katika kiwango kizuri, barabara ya Kibaoni – Kasambya – Mutukula – Minziro iko katika hali nzuri, barabara ya Bukoba Mjini – Mutukula iko katika hali nzuri. Kwa hiyo, hii ni kazi nzuri ambayo TANROADS mnafanya, tunachoomba ni maboresho na kuhakikisha kwamba sasa tunaboresha kutoka katika hatua tuliyopo kwenda katika hatua nzuri zaidi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe maombi kwa ajili ya Wanamisenyi na Wanajimbo la Nkenge. Suala la kwanza Mheshimiwa Waziri, Profesa Mbarawa pamoja na Wasaidizi wako, Mheshimiwa Rais alifanya ziara Mkoani Kagera na akatembelea Wilaya ya Misenyi. Tukamuomba barabara ya Katoma – Bukwali, kilometa 35.7. Ni miaka 10 mpaka leo inajengwa, mpaka sasa hivi imejengwa takribani kilometa saba. Kila mwaka tunajenga mita 200, mita 500 Mheshimiwa Rais aliwapa matumaini mazuri Wanamisenyi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, sasa kama ulitembea mara moja Wilaya ya Misenyi ukatupatia kilometa 25, hizi kilometa 35 ambazo umeshaanza kujenga zinakwama wapi? Nikuombe kwa bajeti hii ya mwaka huu tupatie angalau nusu ya kilometa za barabara ile ambayo ni kilometa 35, tukipata 17 mwaka unaokuja tukamaliza ili sasa tuweze kuomba barabara nyingine za lami za Amshonye kwenda Ruzinga au kutoka Kasambya kwenda Minziro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi najua hilo liko ndani ya uwezo wako, nikuombe sana katika eneo hili muweze kulifanyia kazi. Kwa sababu ukiangalia hata Hansards za Bunge, michango yangu yote katika Wizara yako kila siku tunaongea barabara hii. Mheshimiwa Profesa Mbarawa na wasaidizi wako, najua hili liko ndani ya uwezo wako. Ninakuomba baada ya kumaliza hii bajeti Jumatano mimi nitakuwa mteja wako wa kwanza ofisini kwako ili tuyajenge ili tuhakikishe kwenye orodha ya barabara ambazo kidogo umetengea bajeti, tuweze kuwa na bajeti ya barabara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kwamba barabara ya Kyaka – Katoro – Ibwera na Kyetema. Barabara hii ambayo inaunganisha Wilaya ya Misenyi na Wilaya ya Bukoba Vijijini kwa Kaka yangu, Mheshimiwa Dkt. Jasson Rweikiza imeshafanyiwa usanifu. Tukuombe sana, ukitoka Kyaka – Katoro – Ibwera mpaka Kyetema ni barabara ya muhimu na ukiangalia katika barabara zako, barabara ambayo kidogo imechoka kuliko zote ni barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, kwa hiyo kwa niaba ya wananchi wa Misenyi, lakini naunganisha na wananchi wa Bukoba Vijijini, nikuombe sana eneo hili uweze kulizingatia ili barabara yetu ipate uwezeshaji na iweze kufanya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine kwa niaba ya wananchi wa Misenyi ni barabara ya Mpakani, Mutukula mpaka Makao Makuu ya Mkoa. Mheshimiwa Waziri, hii ni barabara ya lami unaijua, inapitika, lakini inahitaji maboresho makubwa. Tunajua kwamba barabara hii iko katika mpango wa barabara za East Africa, lakini Mheshimiwa Waziri, ni miaka mingi barabara hii imekuwa kwenye programu hiyo. Kama ikionekana kwamba huu utaratibu wa barabara za East Africa kujengwa, basi Mheshimiwa Waziri tukuombe utafute mafungu mengine ili barabara ya Mutukula ambayo inapita kata za Nsunga, Kasambya, Kyaka, Bugorora mpaka kuja Bukoba Mjini iweze kujengwa kwa kiwango cha Afrika Mashariki na iweze kuwa katika standard inayotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri lakini kama tunaona sasa utaratibu huo uko mbali basi nikuombe barabara ile ni uso wa nchi ukiwa unatokea Uganda, hiyo inaonesha sura ya Tanzania kwa wenzetu wanaotoka Uganda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukiangalia jinsi barabara ilivyo, basi tuiboreshe tuweke na taa za barabani kutoka Mutukula kupita Nsunga – Kasambya – Kyaka – Bugorora – Mushasha mpaka Bukoba Mjini, nafikiri inaweza ikawa na image ya nchi, mtu akiwa anaingia Tanzania anaona kweli hapa ni eneo ambalo ni Tanzania kwa sababu barabara zake zote ni nzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, katika barabara hii wananchi wale ambao barabara hii ya East Africa itajengwa walisimamishwa kwa sababu maeneo yao yalichukuliwa kwa ajili ya upanuzi wa barabara mpaka leo wananchi hawajalipwa fidia. Sasa wananiuliza Mbunge, je, tuendelee na shughuli zetu au tusubiri barabara inakuja?

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Prof. ninakuomba sana, kwa sababu nakuaminia, wakati wa kuja kuhitimisha utuambie kama tuendelee kusubiri tunasubiri, subira yavuta kheri. Lakini kama hilo wazo halipo basi Mheshimiwa Waziri nikuombe sasa uweze kuleta majibu ambayo yatatusaidia sisi wananchi wa Misenyi kuwa na jibu ambalo ni sahihi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, suala lingine ni suala la barabara ya Mutukula – Minziro. Nimeshukuru kama nilivyosema mwanzoni. Lakini katika eneo hili, kama nilivyosema, speed yake siyo nzuri na uwezeshaji unakuwa siyo mzuri, nafikiri bajeti siyo nzuri. Mimi niombe, kati ya vitu ambavyo nitaomba kuja ofisini kwako Jumatano baada ya bajeti, baada ya barabara ya Katoma – Bukwali basi na hii barabara ya Mutukula – Minziro ili uweze kuliangalia kwa mapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri, ombi la Wanamisenyi na Wanakagera kwa ujumla lingine ni Uwanja wa Ndege wa Kimataifa Kajunguti. Hili tumekuwa tukilichangia, lakini Mheshimiwa Waziri, kwa weledi wako unafahamu sekta yako yote ya uchukuzi na ujenzi. Unajua kwamba uwanja huu ni uchumi mkubwa wa Mkoa wa Kagera na nchi yetu kwa ujumla. Unajua kwamba uwanja huu unaunganisha nchi yetu na Nchi sita za Uganda, Kenya, South Sudan, Rwanda na Burundi na hii itainua uchumi wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua kwamba sehemu hii, uwanja huu, wananchi walizuiliwa kuendeleza maeneo yao ili kupisha uwanja ni miaka mingi Na gharama za uthamini zilishafanyika. Mheshimiwa Waziri, nikuombe, wakati unakuja kuhitimisha basi na huu Uwanja wa Kajunguti uutolee neno tuone kwamba unakuja kuanza kujengwa au wananchi wanapewa fidia au uthamini unarudiwa upya? Tunaloomba kwa Wanakagera ni kuona uwanja huu unaanza kujengwa au basi hatua za awali zinaanza kwa ajili ya kujenga uwanja huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine la Wana-Misenyi ni kuona barabara zile zote ambazo ziko katika mpango wa matengenezo, ziendelee kutengenezwa. Vile vile kuna barabara ambazo zinazilisha hizo barabara zako ambazo zinaunganisha kwenda mpaka mpakani mwa nchi ya jirani. Kwa mfano, tukiangalia barabara ya Abunazi kwenda mpaka Kakunyu, kuna sehemu ambayo barabara hiyo inaenda inapita Mugango mpaka mpakani mwa Uganda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo barabara ambazo zinaunganisha nchi nyingine ni za kwako, lakini ziko chini ya TARURA ambazo zimekuwa hazitengenezeki. Sasa wewe unatengeneza kipande cha nyuma chote vizuri, lakini kwa sababu bajeti haitoshi, ile barabara ya Bugango kwenda mpaka mpakani mwa Uganda, inakuwa iko katika kiwango kizuri. Pamoja na kwamba ni jukumu letu kuomba upandishwaji wa hadhi wa barabara hizo, lakini naomba kupitia ofisi yako na hilo ulione kwa sababu wewe unaunganisha Taifa na Mataifa ili barabara hiyo iweze kutengenezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi lingine ambalo ni la kitaifa lakini linagusa maeneo mengine ambayo nimeona hapa Dodoma, Mheshimiwa Waziri niwapongeze sana kwa ujenzi wa reli ya mwendoksi ambayo inaendelea vizuri, lakini wakati reli inajengwa kuna maeneo ambayo yalichukuliwa ambayo ni sehemu ya miundombinu ya barabara ambayo iliziba wale watu ambao walikuwa wanahudumiwa na hizo barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nikiangalia katika eneo la Dodoma hapa, nikianzia Njedengwa na Kisasa juu kote ambapo barabara yenu ya SGR inapita, sasa maeneo hayo, pembeni mlijenga barabara ambayo ilikuwa inasaidia miundombinu ya magari ambayo yalikuwa yanajenga barabara ya mwendokasi, lakini sasa hivi mmeziba. Nimeona mmeweka poles, mnaziba. Sasa wale wananchi unakuta kulia ana nyumba, kushoto ana nyumba, barabara aliyokuwa anatokea ni hii ya mbele ambayo sasa hivi unaweka uzio na kuweka fence.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua sheria ipo ndiyo mnayoisimamia, lakini naomba busara sasa itumike katika eneo hili ili wananchi hao, hii barabara ambayo ilitumika kipindi cha ujenzi, bila kuathiri miundombinu yetu ya SGR basi mweze kuona jinsi ambavyo mnaweza kuruhusu wananchi wakaitumia.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. Ninaunga mkono hoja. Ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi kuchangia katika Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na niungane na wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayoifanya na hasa katika uendeleza sekta hii ya ujenzi na uchukuzi na kuhakikisha kwamba miradi yetu yote inaendelea kutekelezwa kwa speed kubwa na kuhakikisha kwamba hakuna mradi unaosimama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite katika maeneo kama manne; nitaongelea barabara katika Jimbo langu la Nkenge, Wilaya ya Misenyi, nitaongelea uwanja wa ndege wa Kajunguti, lakini nitaongelea maboresho ya TPA na mwisho nitamalizia na TRC.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nimpongeze Mheshimiwa Waziri Profesa Makame Mbarawa kwa ziara za mara kwa mara katika Jimbo la Nkenge, Wilaya ya Misenyi. Si muda mrefu ulikuwa kule kukagua ujenzi au maendeleo ya ujenzi wa Daraja la Kitengule, lakini si wewe peke yako umetuma wasaidizi wako Engineer Kasekenya amekuja na ninafikiri na Mheshimiwa Mwakibete yuko safarini kuja tena. Lakini Mheshimiwa Waziri nikushukuru pia ulipotembelea pale ulituahidi kilometa 25 kutoka pale Kibaoni Bunazi kwenda mpaka pale Kagera Sugar. Mimi nakupongeza sana na wana Misenyi wanakushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wilaya ya Misenyi inazo barabara sita ambazo zinahudumiwa na Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi na zenyewe barabara ya kwanza ni Katoma - Bukwali ambayo inatuunganisha na nchi ya Uganda, lakini barabara ya pili ni Mutukura kwenda Minziro ambayo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais, lakini barabara ya tatu ni Kasambia - Nyabihanga kwenda mpaka Minziro tena, lakini barabara ya nne ni Kibaoni kwenda Kagera Sugar mpaka Kakunyu, lakini tunayo barabara ya tano ambayo ni Kyaka kupitia Katoro kwenda Ibwera kwenda mpaka Kanazi hiyo ni barabara ambayo inaunganisha Jimbo la Nkenge na Jimbo la Bukoba Mjini kwa wajomba wangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara hizi nishukuru kwamba zimekuwa zikitengenezwa katika kipindi cha mwaka kwa utaratibu wa periodic maintenance ambazo zimekuwa zikipitika, lakini niombe kusema katika eneo la barabara ya Kyaka - Katoro kwenda Ibwera mpaka Kihetema imekuwa ikifanyiwa usanifu na nimeambiwa kwamba usanifu umekamilika, lakini nimwombe Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake hii barabara sasa imefikia wakati kuanza kutengenezwa kama ahadi inavyosema ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tunayo barabara ambayo aliahidi Mheshimiwa Rais ya Mutukura kwenda mpaka Minziro, nisikitike kusema kwamba kila siku tulikuwa tukiahidiwa kwamba barabara itaanza kutengenezwa na Mheshimiwa Waziri umetuma msaidizi wako Engineer Kasekenya amefika pale na nafikiri alifungashiwa na senene akaja nazo, lakini mpaka leo hatuoni matokeo yanayoendelea pale. Wananchi kule hawaelewi, wanasema viongozi wetu ni kweli wanatupenda wanakuja kwenye ziara lakini mbona hatuoni matokeo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa msisitizo mkubwa niongelee barabara ya Katoma kwenda Bukwaya, barabara hiyo ilianza kujengwa kwa kiwango cha lami mwaka 2011. Mpaka leo ni kilometa saba tu ambazo zimejengwa barabara hiyo ina urefu wa kilometa 39.8 kila mwaka tunapata mita 500, mita 800 nikangalia hesabu za mita 500, mita 800 maana yake tunachukua miaka 50 kukamilisha hiyo barabara.

Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wako tunaomba Wanamisenyi muwaangalie kwa jicho la pekee, barabara ziko nyingi ambazo tungeomba ziendelee kujengwa kwa kiwango cha lami lakini hata moja ambayo imeanza mwaka 2011 miaka karibu 12 kilometa saba. Mimi naomba kwa kweli Serikali sikivu ya Mheshimiwa Mama Samia ione kwamba Wanamisenyi wanahitaji hiyo barabara, imalizike sasa ili tuweze kwenda katika barabara nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na juhudi kubwa wanazozifanya wataalam wetu wa mkoa tunaye Meneja wetu wa Mkoa Engineer Sanga Msangi, lakini na msaidizi wake Engineer Ntuli, wanafanya kazi nzuri, wanawasiliana na mimi vizuri, lakini shida ni uwezeshaji. Leo katika mwaka huu katika bajeti tunazo mita 800, na nimeona katika ukurasa wa 352 umeniwekea kilometa 1.5; Mheshimiwa Waziri wewe unatengeneza mabarabara makubwa kilometa nyingi sana kwa nini hiyo kilometa 1.5 mita 800 mpaka miaka 50 wote hatutakwepo mimi na wewe ndio barabara itakamilika. Nikuombe sasa leo katika bajeti hii angalau tenga nusu kilometa 17 mwaka ule unaokuja kilometa 17 tunamaliza tunahamia barabara nyingine. Mimi nakuamia Profesa na haujawahi kushindwa kwa hiyo naamini utalitekeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niongelee ujenzi wa uwanja wa Omukajunguti; kwa nia njema Serikali iliona kuna haja ya kujenga Kajunguti International Airport na uwanja huu mahususi ulikuwa ni kwa ajili ya kuhudumia nchi za Maziwa Makuu ya Afrika nchi kumi, tunayo Malawi, Zambia Msumbiji, Uganda, Rwanda, Burundi na Tanzania lakini katika eneo hili ilikuja likaainishwa eneo, wananchi wakazuia kuendeleza na wananchi wakatulia kwa upendo mkubwa wakijua kwamba tunaletewa uwanja wa ndege, uwanja wa ndege huu ukainue uchumi wa Mkoa wa Kagera.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo Mkoa wa Kagera tukiangalia GDP yetu tuko wa mwisho katika mikoa yote 26 ni kwa sababu hatuna miundombinu na mawasiliano ya kuweza kusafirisha bidhaa zetu, kuuza ndani ya nchi na nje ya nchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Mkoa wa Kagera Mheshimiwa Waziri hata jirani yako Mheshimiwa Waziri Ndaki hapa anajua kwamba Mkoa wa Kagera ndio una ranchi kubwa za mifugo. Kwa hiyo tunao ng’ombe, lakini ng’ombe hao hawana thamani leo kwa sababu hatuwezi kufanya export, hatuwezi kuanzisha viwanda, hata mwekezaji wetu wa kiwanda aliyepo pale Karagwe kwa ndugu yangu Bashungwa ameshindwa kuendelea kwa sababu hana jinsi ya kusafirisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe sana uwanja huu ni wa muhimu sana kwa ajili ya kuhakikisha unainua uchumi wa Mkoa wa Kagera; tuuze, tuanzishe viwanda vya kusindika mazao mbalimbali, tunalima vanilla, tunalima maparachichi, lakini wananchi wanakata tamaa kwa sababu hawana jinsi ya kusafirisha maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika eneo hilo niombe kusema kwamba tunao uwanja kweli wa Bukoba ambao unaendelea sasa hivi, lakini uwanja huo ukiangalia runway ile ni kilometa moja na nusu, na ninyi ni mashahidi mnajua specification za ndege; Bombadier Q400 minimum runway ni kilometa 2.2 watu wote shuhudia na Mheshimiwa Waziri ukitua Bukoba rubani wako anavyoshika break ni tofauti anaposhika kwenye sehemu nyingine ila tunaendelea kuvumilia tukiwa na tumaini sasa Omukajunguti inakuja kujengwa ili sasa iwe ni suluhisho kwa wananchi wa Misenyi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuponge juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali hasa upande wa uboreshaji wa bandari yetu, tumeona kwa kweli gati zimejengwa sana meli zinaendelea kuja kushusha mizigo, ni maendeleo makubwa na lazima tusifie Serikali yetu kwa sababu yanayofanyika tunayaona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hayo tu niipongeze Serikali ya Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan, kuna eneo ambalo lilikuwa pale karibu na bandari yetu la EPZA ambalo lilikuwa linasababisha magari yanayoingia bandarini na kuzuia wananchi wanaoenda Kigamboni, huwa inaleta foleni kubwa na kudololesha huduma zinazotolewa pale bandarini, lakini Serikali ya Mama Samia imetoa eneo hilo kwenda katika uongozi wa bandari yetu na hivyo limetengwa katika umahususi kuweza kutunza baadhi ya makontena na shughuli zingine. Kwa hiyo niendelee kumpongeza Mheshimiwa Rais, lakini pia nimpongeze Mkurugenzi Erick kwa kazi nzuri pamoja na timu yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa ufupi niongelee pia TRC nimpongeze Mheshimiwa Rais, wakati anaingia katika Awamu yake ya Sita alikuta kuna lots mbili ambazo zimeanza kutengenezwa, lakini leo tunaongelea lots tano zimeongezeka lots nyingine tatu, tumeongezeka Makutupola – Tabora; Tabora – Isaka; na Isaka - Mwanza, na Tabora - Kigoma iko katika hatua mbalimbali za manunuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni suala la kumpongeza sana Mheshimiwa Rais, kwa hiyo na hii nimpongeze Mheshimiwa Waziri na wasaidizi wake kazi nzuri mnaifanya. Kwa hiyo niwaombe sana muunganiko wa hizi lots zote zikikamilika tukienda Tabora - Kigoma maana yake tuna uwezo wa kufanya biashara na DRC Congo na Burundi na hivyo uchumi wa nchi utaendelea kuongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme kwamba tumeona maboresho ya reli ya zamani, Mheshimiwa Waziri lazima tukupongeze na hilo, kuna reli ambazo zililala muda mrefu lakini zilifufuliwa kuanzia Serikali ya awamu ya tano mpaka leo tunaona Dar - Moshi, Moshi - Kilimanjaro na sehemu zingine na hizo zimeweza kuongeza pia na mapato ndani ya taasisi yetu ya TRC. Kwa hiyo nimpongeze na ndugu yetu Bwana Kadogosa kwa kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Serikali katika maeneo ya mikataba na hasa Serikali katika kuingia katika mkataba wa Fixed Lump Sum Contract, huu ni mkataba wa jumla usiobadilika katika mabadiliko ya corona, katika bei za mafuta, kama tusingekuwa na mikataba ya namna hii maana yake tungetengeneza hasara kubwa zaidi ya matrilioni ya pesa, lakini Serikali yenye maono na wataalam na wazalendo wameweza kuliona hili kwa mbali na kuweza kuzuia hasara ambayo ingeweza kutokea.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele yako ya pili ilikuwa imelia.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuunga mkono hoja naomba sana Mheshimiwa Waziri hasa kwa Wilaya ya Misenyi paangalie, ahsante sana na nakushukuru. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi, niungane na wenzangu kuwapongeza Mheshimiwa Mohamed Mchengerwa na Mheshimiwa Deo Ndejembi, kwa kuaminiwa na Mheshimiwa Rais.

Naomba niongee machache kwa sababu ya muda, lakini pia niwaombe Mheshimiwa Waziri na Naibu wake naona ni vijana ambao wana kesho nyingi njema na hivyo wakichukua fursa hii ya kupata ushauri na kuiboresha Wizara ya Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora basi tutakuwa na watumishi wenye hali ya kazi na hivyo malengo mahususi ya nchi yetu yataweza kufikiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, najua nitatoa case study katika local government na najua mwongozo ambao unasimamia maadili ya utumishi wa umma ni Kanuni za Utumishi wa Umma za mwaka 2009 yaani Standing Order of 2009.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kujikita kwenye fursa sawa kwa watumishi wote. Halmashauri inazo Idara 18 baada ya moja ambayo ilikuwa Idara ya Maji kutolewa na kuanzishwa Taasisi ya RUWASA. Lakini katika maeneo hayo watumishi wote hawahudumiwi sawa na kanuni za utumishi wa umma. tunaona katika OC inayopelekwa katika Halmashauri hizo suala la leave, suala la likizo zime- concentrate katika baadhi ya idara na idara hizo ni Idara ya Elimu ya Msingi, Elimu ya Sekondari na Afya na huko hazitoshi lakini idara zote zilizobaki hakuna mtumishi anayeweza kukuambia kwamba nilishawahi kulipwa hela ya likizo, hakuna mtumishi anayeweza kukuambia kwamba nilishawahi kulipwa hela ya kusafirisha mizigo kurudi kwetu kutoka kwenye OC. Na idara hizo nyingine OC inaenda shilingi milioni moja Idara ya Kilimo, Idara ya Mifugo, Idara ya Mazingira, Idara ya Mipango. Niombe Wizara iangalie kwa sababu yeye ndio baba, mama wa watumishi wote na Standing Order sasa ya mwaka 2009 iweze kuzingatiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni suala la OPRAS, mimi nimshukuru Mheshimiwa Rais jana ni kama alifungua kifua changu na kunifanya nipumue vizuri baada ya kuiona pia OPRAS ni tathmini ya utendaji kazi ya watumishi kwamba haiko vizuri inatakiwa iboreshwa. Najua kutakuwa na forum mahsusi kwa ajili ya kuchangia vizuri, lakini niombe kushauri tunazo taasisi za Serikali, mimi nishawahi kuwa mtumishi wa TFDA leo ni TMDA iliboresha ile OPRAS tukaingia kwenye TASA - TFDA Staff Appraisal ambayo ilikuwa kwa kweli inatumika hata kumpata mfanyakazi bora wa Mei Mosi anapatikana kupitia hiyo. Lakini leo OPRAS haipo na Mei Mosi mtumishi bora anapatikana kwa zamu, kwamba tupeane zamu, sijui ni nani maaarufu zaidi naomba kwa hiyo niombe sana iweze kuboreshwa kama Mheshimiwa Rais alivyoshauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine nilitaka kushauri kwenye suala la uhamisho. Tumekuwa na utaratibu wa kuhamisha watumishi na tumepewa maelekezo kwamba watumishi wahame kadri inavyowezekana, lakini niombe chain of command, chain ya mawasiliano ya viongozi wetu izingatiwe, yule ambaye tumemkasimu kusimamia watumishi katika eneo lake basi m-consult hata kidogo, leo unakuta Halmashauri imetumia fedha kumuhamisha mwalimu kwa gharama wa sayansi, amefika hapo barua inatoka Utumishi au inatoka TAMISEMI bila taarifa Mkurugenzi kujua. Tunaiweka Serikali katika gharama kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi niombe chain of command mamlaka haipingwi, lakini wasiliana na wale wanaokusaidia kusimamia watumishi kule chini. mtaongea lugha moja na tunajua kwamba kila mtumishi atapata haki yake ya kuhama. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho niungane na hoja ya Mheshimiwa Husna Sekiboko na Mheshimiwa Ndulane, ni watumishi ambao walikuwa watumishi wakaenda kugombea katika nafasi za siasa. Katika eneo hili lilikuwa na ukakasi na grievance nyingi sana, mimi niwaombe Wizara hii ilifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna post nyingine ni political post akimaliza anapewa gratuity yake, anafungasha, anaondoka, lakini post nyingine kama walivyosema za Wakurugenzi na watumishi wengine zilikuwa ni za kiutumishi, wamepewa ajira, wamethibitiswa kazini na walipoondoka walitakiwa sasa wapangiwe vituo vingine na hii tumeiona, hata kipindi cha nyuma wapo Ma-RAS ambao walitolewa kazini, wapo Wakurugenzi walitolewa kazini, lakini walipangiwa RS, wapo wanafanya kazi na taasisi nyingine za Serikali wengine wameletwa katika Wizara zenu. Kwa hiyo, tuombe hao wenzetu ambao wapo mtaani, wanazurura hawajui la kufanya, niombe sasa Wizara ifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi na mimi niungane na wenzangu kupongeza Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na vyombo vyake kwa ulinzi mzuri wa nchi yetu. Tunajua tunajivunia tunu za Taifa na mahsusi kwenye upande wa amani tunajua Wizara ya Mambo ya Ndani pamoja na vyombo vyake wanachangia sana katika eneo hilo.

Mheshimiwa Spika, pamoja na pongezi hizo kuna mambo kadhaa ambayo yanahitaji kuboreshwa ndani ya Wizara yetu hiyo ili ustawi wa wananchi uweze kuwepo katika sehemu mbalimbali za nchi yetu. Najua ni bahati kwa nchi au mkoa kuwa na ujirani na nchi zingine. Kwa mfano, Mkoa wa Kagera tunapakana na nchi tano; Uganda, Rwanda, Burundi, DRC na Sudan Kusini. Hata hivyo, wananchi wa Mkoa wa Kagera wamekuwa ni wahanga na hasa katika kutambuliwa na kupewa Vitambulisho vyao vya Taifa ili waweze kupata huduma zingine ambazo wanastahili kupewa kwa mfano kusajili simu zao. Pia tumeona Wizara ya Kilimo imekuja na utaratibu wa kusajili wananchi kulipwa fedha zao kupitia simu zao, huduma hizo wamekuwa wakizikosa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia Wilaya ya Misenyi, Kyerwa, Karagwe, Ngara wote tumekuwa wahanga wa kukosa vitambulisho na wananchi wanaishi kwa tabu kama vile hawapo ndani ya nchi yao. Suala hili limesababisha Mkoa wa Kagera ukadorora katika maendeleo. Mtu hawezi kufanya kitu kizuri, hawezi kulima shamba zuri, hawezi kujenga nyumba nzuri kwa sababu kesho ataambiwa wewe siyo raia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nijikite sana kwenye Wilaya ya Misenyi ambapo ndiyo jimbo langu. Kuna familia baba ameambiwa siyo raia, mama ni raia, mtoto wa kwanza ni raia, wa pili siyo raia. Sasa mpaka tunaleta mtafaruku katika familia, watu wanaenda kutafuta hata vinasaba maana baba anamuuliza mama huyu sasa ambaye siyo raia ni wa nani?

Mheshimiwa Spika, kwa Wilaya yetu ya Misenyi ukitaka kumpima mwananchi kwa kuongea Kiswahili au kuimba Wimbo wa Taifa sisi wote siyo raia. Hii ni kwa sababu mimi naongea Kihaya, Mnyankole akiongea Kinyankole tunaelewana bila shida. Sasa unaponipima kwa kusema kwamba niongee Kiswahili au niimbe Wimbo wa Taifa, hatuwatendei haki. Sisi wote ni mashahidi tukipangana kwenye mstari kila mmoja umpime anaimba Wimbo wa Taifa mpaka mwisho kuna wengine watateleza katikati, sasa hicho ndiyo kipimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote ni mashuhuda Wilaya ya Misenyi umekuwa ni uwanja wa vita ya Uganda na Tanzania. Sisi ndiyo tulikuwa wahanga, mwingiliano wa kabila mbalimbali kutoka Uganda umekuwepo na tukaishi kama jamii moja. Sasa leo kigezo cha Wizara cha kusema kwamba imba Wimbo wa Taifa, ongea Kiswahili, watu wanaongea Kinyankole, Kihaya, tunaongea Kiganda vizuri kabisa na wao wanaongea hivyo hivyo. Kwa kweli suala la vitambulisho katika Wilaya ya Misenyi kwa kweli limekuwa ni janga la kitaifa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na kwamba wameanza kujitahidi wanapata namba, hivi kinachoshindikana ku-print kale kakadi ni nini? Tumekuwa kwenye halmashauri kule tuna- print kadi za wazee za bima za afya kuna mashine Sh.25,000, una-print vile vitambulisho unampa mtu anaendelea na maisha yake. Ile namba ukishaingiza kwenye computer kule kwako unakotaka itasoma, lakini hata kitambulisho kile ambacho unaweza ku-print kwa Sh.200, kwenye Wizara yetu imeshindikana, shida ni nini?

Mheshimiwa Spika, wananchi wetu wamepata shida sana kuhusiana na jambo hili. Cha ajabu wakati wa uchanguzi wote ni raia lakini ikija kwenye kuwatambua kama Watanzania siyo raia. Mimi wamenituma, kupitia Kiti chako watuambie kama sisi siyo raia tupelekwe kwenye nchi ambayo tunastahili twende kuishi huko. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naamini Watanzania ndiyo wanatakiwa kufaidi maziwa na asali ndani ya nchi yetu. Sasa kumwambia Mtanzania halisi kwamba hajaongea Kiswahili, Kiganda, Kihaya hicho siyo kipimo. Waende waangalie maana zile kaya zipo. Ukienda kule kwetu Bukoba sisi tunapojenga boma ni kama uwanja wote huu wa ofizi za Bunge, ni mtu ana mji wake na migomba yake imemzunguka, ukivuka hapo unaenda mji mwingine tunahesabika kirahisi, mtu yupo tangia mwaka 1920 leo uamwambia siyo raia? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pamoja na kazi nzuri wanayofanya Wizara ya Mambo ya Ndani kwenye eneo hilo bado hawajafanya vizuri. Hii inasababisha wakati mwingine majeshi yao wanaitumia kama loophole kwamba nikuite raia au siyo raia, unasemaje? Kwa hiyo, niombe sana Wizara ya Mambo ya Ndani ilichukulie kwa uzito suala hili ili wananchi waweze kuwa na raha katika nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maji
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi na niungane na wenzangu kupongeza Wizara ya Maji chini ya uongozi mahiri wa Mheshimiwa Waziri Awesso, Mheshimiwa Naibu Waziri, Eng. Maryprisca lakini pia na Watendaji Wakuu, Katibu Mkuu Eng. Sanga na Naibu Katibu Mkuu mama yetu Nadhifa Kemikimba lakini pia na Mkurugenzi Mkuu wa RUWASA na Mameneja wote wa Mikoa na Wilaya zetu kwa kazi nzuri ndani ya halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa utaratibu wa binadamu asiyeshukuru kwa kidogo hata kikiwa kikubwa hawezi kushukuru. Nishukuru Serikali kupitia Wizara ya Maji kwa miradi mikubwa ya maji ambayo wametupatia ndani ya Wilaya ya Misenyi, ambapo tunao mradi wa Gera milioni 570 ambao umekamilika katika vijiji vitatu na sasa hivi nikushukuru sana Waziri kwa kutupatia extension katika vijiji vingine viwili vya Kashaka na Kashekya. Kwa hiyo, maana yake katika eneo hilo vijiji vyote vitakuwa vimefikiwa kwa kupata maji kutoka kwenye Mradi wa Gera.

Mheshimiwa Spika, lakini pia, wananchi wa Misenyi wanakushukuru pia kwa mradi mkubwa wa maji wa Kyakabulanzi wa bilioni 15.1 ambao tumeendelea kufuatilia unavyoendelea kujengwa na upande wa mkandarasi hela zimeendelea kwenda kwa kiasi lakini pia na upande wa force account kutumia wataalam wetu nimeambiwa vifaa vimeendelea kupelekwa. Kwa hiyo, tukushukuru lakini tuombe basi uwezeshaji uendelee ili uweze kukamilika wananchi wa Kyaka, Kasambya na majirani pale waweze kupata maji.

Mheshimiwa Spika, niendelee kushukuru kwa bajeti ya mwaka 2021/2022 kwa miradi ambayo kutoka katika wilaya yetu imeweza kupitishwa na Wizara. Na tunaona katika maeneo mbalimbali miradi ya mradi wa maji katika eneo la Kashenye na Bushago na Bukwali tumeweza kupata fedha kiasi kwa ajili ya kupata maji lakini tumeona mradi wa Kitobo Katolelwa, Byemagwe, Byeju na Byamtemba yote imeweza kupata lakini na uchimbaji wa visima saba katika vijiji mbalimbali na kutanua mradi wa Kashaba.

Mheshimiwa Spika, ombi langu kwa Wizara ya Maji ni kuomba kwa kazi nzuri ambayo mmeshaifanya tayari, kuna miradi ambayo katika mwaka huu wa bajeti ambao unaisha tarehe 30 Juni, ilikuwa aidha ipo kwenye pipe line au imeshafanyiwa hatua za awali. Kwa mfano, tukiangalia katika eneo la Rwamachu na Rutunga Wizara mmechimba visima na wananchi wameshangilia kuona maji mengi yanatoka. Kwa hiyo, ni matarajio yao kwamba baada ya vile visima kuchimbwa tulikuwa tunaona hatua ya pili sasa ni kupeleka maji yawafikie wananchi.

Mheshimiwa Spika, lakini katika hii bajeti sasa 2021/ 2022 tunaona kwamba tumeacha nyuma. Niombe Mheshimiwa Waziri najua bajeti sio kubwa sana tunagawana kilichopo, lakini basi wananchi wa Rwamachu na Rutunga waweze kuona sasa mradi unawafikia. Lakini sambamba na hiyo, Wizara imechimba visima katika kijiji chetu cha Ruano na Nyalugongo na yenyewe visima tayari vimechimbwa. Kwa hiyo, tungefarijika kuona sasa baada ya uchimbaji na wananchi kujitoa kwa ajili ya kushirikiana na Wizara na kuona maji yanawafikia basi, ndani ya bajeti hii ya 2021/2022 na eneo hilo liweze kuwekewa umakini ili bajeti iweze kutengwa wananchi hawa wapate maji.

Mheshimiwa Spika, lakini niombe kumkumbusha pia Mheshimiwa Waziri katika Kijiji chetu cha Kashasha chanzo kipo ni mradi wa Mbale ni extension ya kujenga matenki na kusambaza maji wa mserereko kwa wananchi wa Kijiji hicho cha Kashasha ili waweze kupata maji. Na katika bajeti ya mwaka huu ambao unaisha tarehe 30 Juni ilikuwa imetengwa hela kadhaa kwa ajili ya kuhakikisha kwamba mradi huo unafanikiwa. Kwa hiyo, nikuombe sana Wizara yetu ya Maji iweze kutusaidia katika maeneo hayo kwa kiasi kikubwa naamini, kama miradi hii itatekelezwa ndani ya Wilaya ya Misenyi angalau upatikanaji wa maji utakuwa umefikia takribani asilimia 72 au 75.

Mheshimiwa Spika, lakini tunaendelea kushukuru kwa kuanza maandalizi ya miradi mbalimbali katika Kata yetu ya Minziro kwa Vijiji vya Minziro, Kalagara na Kigazi. Naamini na wananchi hao baada sasa ya upembuzi ukikamilika na vijiji vingine vya Rwamashonga lakini tumeona Mwemage kote kazi inaendelea pamoja na Kyazi. Niombe sana kuungana na wenzangu suala ambalo limekuwa likitatiza kidogo kwenye miradi yetu ya maji na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuombe Wizara kwa juhudi kubwa ambazo imeendelea kufanya na sisi kama kuna vikwazo vingine basi, ni kuliambia Bunge Tukufu kusaidia hasa cash flow ya miradi ambayo tayari iko kwenye pipe line inaendelea. Naamini kama fedha zikiwa zinakuja kwa wakati ingesaidia sana Wilaya fulani haivuki ikiwa na miradi viporo kwenda katika mwaka wa fedha unaofuata. Ikishavuka miradi haijatekelezwa na ilikuwa kwenye bajeti iliyopita inakuwa ni shida kidogo, maana yake mwaka ujao tunategemea tupate sasa miradi mipya kuliko hii ya nyuma ambayo haikutekelezwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tuombe sana kwa juhudi kubwa mnazozifanya tuna Imani na Wizara kwa utendaji kazi wa Waziri na Wasaidizi wako wote, tunaamini haya yote yataweza kutendeka na wananchi wataendelea kupata maji na tutafikia asilimia zile ambazo zinaendana na sera ya maji katika vijiji na miji na tupate maji safi na salama.

Mheshimiwa Spika, kwa Wilaya ya Misenyi niseme wananchi wanafarijika sana na kwasababu, vyanzo vya maji ni vingi tunaendelea kupata matumaini hayo.

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru sana naunga mkono hoja, ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Mifugo na Uvuvi
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu ya Mifugo na Uvuvi. Kwanza, nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa nia njema ya kutaka maendeleo katika ufugaji, uvuvi na maendeleo kwa ujumla katika Wizara hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nafasi ya pekee nimpongeze sana Waziri, Mheshimiwa Mashimba Ndaki; Naibu Waziri, Mheshimiwa Abdallah Ulega kwa kazi nzuri mnayoifanya kwa kushirikiana na Katibu Mkuu, Tixon Nzunda, Naibu Katibu Mkuu; Wakurugenzi wote wa Wizara; watumishi wote wa Wizara ya Mifugo na Uvuvi na Taasisi zake, mahsusi pia na watumishi wote wa Halmashauri 184 ambao wanasimamia eneo hili la Wizara ya Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe pongezi za dhati kwa Mheshimiwa Rais kupitia wizara yetu hii kwa Wilaya ya Misenyi kututengea milioni 350 kujenga mnada wa mpakani boarder market na sasa hivi mnada huo unajengwa kwetu ni faraja kwa sababu utainua uchumi wa wana Misenyi uchumi wa wana Kagera lakini pia na soko la mifugo ndani ya Mkoa wa Kagera litakuwa limepatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niongelee kidogo kuhusiana na mazingira ya upangishaji katika Ranchi zetu za Taifa kupitia NARCO, kwanza kwa nafasi ya pekee nimpongeze Meneja wa NARCO Profesa Peter Msofe pamoja na watumishi wote wa NARCO kuanzia ngazi ya Taifa lakini mpaka ya ranch wanaposimamia katika maeneo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Kagera ni mkoa ambao una Ranchi nyingi kuliko mikoa mingine yote nchini Tanzania, tunazo Ranchi sita tunayo Kagoma, Kitengule, Kikukura, Mabale, Mwisa na Misenyi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ukiangalia wingi wa Ranchi hizi maana yake idadi ya mifugo ambayo iliyoko Tanzania mingi imekuwa based katika Mkoa wa Kagera. Lakini cha kushangaza Mkoa wa Kagera ni mojawapo mkoa maskini kuliko mikoa yote Tanzania kwa taarifa za GDP ambazo zimetolewa na sababu zake ni nini ambazo zimetolewa na sababu yake ni nini kama alivyosema kaka yangu Mheshimiwa Mwijage ufugaji unaoendelea ndani ya ranchi zetu ni uchungaji na sio ufugaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ambayo sio malengo mahususi ya Serikali tukijiringanisha na nchi jirani Uganda sisi tunafanya kazi kwa ushirikiano na wenzetu wa Uganda, tunatembeleana kuangalia anachofanya mwezetu wa Uganda na wanachofanya watanzania, katika nchi ya Uganda hatuongelei ukubwa wa eneo hatuongelei uwingi wa idada ya mifugo tunaangalia productivity katika eneo ulilonalo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unaangalia mfugaji ndani ya nchi ya Uganda anazo heka 400 tu mle ndani ana ng’ombe 150 productivity inayotoka katika eneo hilo ni kubwa kuliko mfungaji wa Tanzania ambaye ana hekta 6000 ana ng’ombe 1000, wapi tunakwama?

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kuwapenda wafugaji wetu, kupitia NARCO wamekodisha kwa utaratibu mzuri wanaandika business plan lakini kuna mambo ambayo kama Taifa kama Serikali tunahitaji kuyasimamia ili hawa wafugaji sasa ndani ya Ranch zetu wawe wafugaji kweli na sio wachungaji. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la kwanza, zipo changamoto mbalimbali katika eneo hili ambazo ziko silent kwa Serikali yetu au kama inazifanyia kazi basi si kwa kiwango kile ambacho kingeweza kuwasaidia wafugaji wetu wakapiga hatua kubwa. Suala la kwanza tunalo suala la wizi katika ranchi zetu wizi ni mkubwa sana na wizi asilimia 90 mifugo inaibiwa kwenda nchi za jirani kama mnavyojua Mkoa wa Kagera tumepakana na nchi zote lakini n’gombe wanaibiwa lakini Wakuu wetu wa Wilaya zinazozunguka mahali pale wanajitahidi kadri wanavyoweza lakini wamewezeshwa kiasi gani na wizara yetu kuhakikisha sasa wanalinda mifugo yetu wanalinda wananchi katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, bajeti ya Ofisi ya Mkuu wa Wilaya tunaielewa lakini hakuna sehemu ambayo toka inatoka wizarani kupeleka katika wilaya zetu ili vyombo vyetu vya ulinzi na usalama viweze kufanya kazi kwa ufasaha, nitafika sehemu ambayo nitashauri hizo fedha zitoke wapi kwenda katika kusaidia vyombo vyetu vya ulinzi na usalama ili wananchi waendelee kufuga.

Mheshimiwa Naibu Spika, tuangalie miundombini mfugaji anatakiwa kuwekwa bwawa anatakiwa kuweka josho ni mfugaji gani wa Tanzania ataweza kununua excavator ang’oe miti yote katika hekta zake alizopewa achimbe mabwawa sasa Serikali inatakiwa kuja na utaratibu ambao inaweza kuwatafutia mikopo kwa kuwapa vifaa, lakini naweza kutafuta vifaa vya Serikali tumeona Wizara ya Ardhi, walinunua vifaa vya kupima Tanzania nzima, ukitaka kupima halmashauri unaenda pale Wizara ya Ardhi wanakupa vifaa unapima halafu unarudisha sasa na Serikali hapa kupitia Wizara ya Mifugo walitakiwa wawe na vifaa kama ni ma-excavator wanayo watu wakitaka kuchimba mabwawa wapewe wachimbe mabwawa halafu watakataka katika hela zinazotokana na uuzaji wa mifugo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini hili halipo inakuwa ni ngumu sana kuelewa ni wakati gani anaweza kufanikiwa. Lakini zipo changamoto za mbegu, dawa za kuongeshea mifugo, chanjo zote hizo ningeomba Serikali ije na majibu ya kuhakikisha kwamba inakuwa na mkakati madhubuti kwamba wananchi wetu basi wanapewa ruzuku au inaweka utaratibu mzuri waweze kufanikiwa katika hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kushauri eneo lingine ni upimaji mpya ambao ulifanyika ndani ya vitalu unajua wakati wa upimaji mpya kuna maeneo mengine Serikali ilisaidia sana kutatua migogoro. Nimwambie Mheshimiwa Waziri kuna maeneo mengine ambapo tumeleta mgogoro zaidi tumechukuwa maeneo ya vijiji yakaingia kwenye Ranch za Taifa, tuangalie kwa mfano ukienda kule kwangu nenda Kijiji cha Bunga utaona vitongoji cha Rwambogo na Shantabwa vyote vimeingia katika Ranch ambapo awali haikuwa hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nenda pale Kakuyu uangalie Kitongoji cha Katangiliza chote kimingia kwenye Ranch ninacho kitalu namba kumi Mheshimiwa Waziri unakijua kiko na kesi lakini kesi ikiisha wananchi wameshaomba hekta 2000 wapeni walime mifugo na wananchi vyote vinategemeana tusipende sana mifugo tukaacha wananchi wakilima na mifugo yenyewe basi inakuwa ni rahisi kuweza kutumia kwa hiyo, niombe kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna suala la uvamizi wa tembo mimi naomba mshirikiane na Wizara yetu ya maliasili na utalii kwa mfano kwenye Ranch za Misenyi na mabahi ni nusu na nusu na ng’ombe. Kwa hiyo, niwaombe sana, kila siku napigiwa simu za kuhakikisha kwamba tunaenda kufukuza hao tembo, Mkurugenzi wangu hana resource za kutosha bunduki sijui tunazo mbili risasi lakini Wizara ya Mifugo ni lini mmetuchangia angalau risasi au bunduki kule hamna naomba tu hiyo inawezekana na wizara inakusanya fedha nyingi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri kidogo kwenye tangazo la GN namba 35 la mwaka 2018 kupitia tozo za minada tunayo minada ya aina tatu tunao mnada wa awali primary market tunao secondary market wa pili tunao na boda. Niombe wizara hii iangalie vizuri eneo hili Wizara ya Mifugo katika ng’ombe mmoja kwa mfano nikiongelea mnada wa boda inachukuwa kibali cha kusafirisha ng’ombe kwenda nchi ya jirani shilingi 25,000 inachukuwa tozo ya ushuru shilingi 4,000 halmashauri inaambulia shilingi 1,000; buku tu Wizara inachukuwa shilingi 29,000.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini ardhi ile iliyoko pale yote ni halmashauri watumishi hata kama wote ni watanzania ni wa wizara wote wako chini ya Mkurugenzi resource anazotumia kwenda kusimamia pale ni za halmashauri elfu moja Mheshimiwa Waziri kitu cha kwanza naomba ukiangalie hicho gawana mapato yale angalau ile elfu nne ya tozo mnaweza mkaigawa katika halmashauri ikachukuwa elfu tatu nyie mkabaki na 2,000 na kibali cha kusafirisha unakuta wewe unachukuwa 27,000 halmashauri inachukuwa elfu tatu itasaidia na hiyo mnaweza mkaitolea maelekezo kamati ya ulinzi na usalama inapata fedha za kwenda kufanya dolia lakini pia majosho yanajengwa kupitia halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe hilo wana Misenyi walinituma kwa dhati niwashukuru kwamba leo mmetuanzishia mnada wa boarder market lakini niombe sasa Serikali kupitia wizara yetu hii mje na majibu kwa wana Misenyi kwamba tunaingia MoU uendeshaji.

NAIBU SPIKA: Ahsante Mheshimiwa Kyombo kengele ya pili.

MHE. FLORENT L. KYOMBO Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi hii, naomba kuunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2023
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii ya kuchangia katika taarifa ambayo imewasilishwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nashukuru na kuipongeza Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan pamoja na Wizara zote ambazo zinasimamiwa na Kamati. Tumeona kazi kubwa ambayo inafanyika katika kipindi cha mwaka mmoja na hizo ni Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na utawala bora; Ofisi ya Rais, Mipango na Uwekezaji; Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano; Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu na Wizara ya Katiba na Sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuangalia nia ya dhati ya Serikali ya Dkt. Samia Suluhu Hassan, tunaona jinsi alivyodhamiria kuishi kwa misingi ya Utawala Bora, misingi ya haki na misingi ya utii wa sheria. Katika kipindi cha mwaka mmoja, Kamati yetu imepitia Miswada 12. Ndani ya Miswada hiyo 12, kuna sheria zaidi ya 74. Kwa kuangalia hivyo, inatuambia nini? Ni kwamba Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amedhamiria kusimamia nchi yake katika mfumo wa Utawala Bora, katika mfumo wa utii wa sheria na katika mfumo wa haki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuishi katika haki hizo maana yake Mheshimiwa Rais anaishi katika Falsafa yake ya 4Rs ya kuhakikisha kwamba maridhiano yamekuwepo, uvumilivu umekuwepo na ustahilivu, lakini pia reforms na rebuilding zinakuwepo katika nchi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona, tumekagua miradi mbalimbali, lakini mahususi nitaongelea miradi miwili, na miradi hiyo yote inalenga kupeleka huduma karibu na wananchi, na pia inalenga kutekeleza haki. Tumeona miradi ya ujenzi wa jengo la Kituo Jumuishi cha Kutoa Hati. Katika eneo hili tunaona katika jengo moja Mahakama ya Mwanzo mpaka Mahakama ya Rufani mwananchi akiingia pale maana yake anapata huduma zake zote. Pia na Watendaji wetu wa Mahakama, maana yake akihitaji faili kama ni rufani, ahitaji kuandika kesi ambayo imeenda katika Wilaya nyingine au kitongoji kingine, zote ziko ndani ya jengo moja. Hiyo imerahisisha utoaji wa haki za kisheria. Kwa hiyo, tunayo kila sababu ya kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake na wasaidizi wake wote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tumeona ujenzi wa Kituo Jumuishi kwa Taasisi za Kisheria. Ukiingia ndani ya jengo moja unamkuta Wakili Mkuu wa Serikali yuko pale, unamkuta Waendesha Mashtaka wako pale, Jeshi la Polisi wako pale, Taasisi zote zinazosimamia sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi siwezi kusema maneno mengine zaidi ya kusema nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya Utawala Bora, nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya utii wa sheria, nia ya dhati ya Mheshimiwa Rais ya haki kwa wananchi wake, tunaiona kwa matendo. Tuna kila sababu pia ya kumpongeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu ya Utawala, Katiba na Sheria inasimamia Wizara tano kama nilivyotaja, na leo nitajikita katika maeneo makubwa ambayo ni Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu na nitaongelea kwa Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano kama muda utaruhusu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu ya kwanza, katika Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera Uratibu na Bunge nitajikita katika Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya. Ni lazima nimpongeze Mheshimiwa Rais na wasaidizi wake katika Wizara hiyo ambao ni Mheshimiwa Jenista Mhagama, msaidizi wake Mheshimiwa Ummy Nderiananga, Katibu Mkuu Jimmy na mahususi, Kamishna Jenerali Ndugu yangu Aletas Lyimo, Makamishna Wasaidizi na Watendaji wote wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Madawa ya Kulevya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa imesomwa hapa tumesikia, ongezeko la matumizi ya Madawa ya Kulevya Duniani ni zaidi ya milioni 200 ambayo ni sawasawa na asilimia nne ya watu wote duniani. Tanzania siyo kichaka, tunaendelea pia, suala hili tunaliona ndani ya nchi yetu, lakini tumekuwa na watumishi ambao chini ya Wizara ya Sera, Bunge na Uratibu chini ya Mamlaka ya Kudhibiti Madawa ya Kulevya wakijituma usiku na mchana, tumeona wanakagua, tunagundua viwanda vya kutengeneza biscuit za madawa ya kulevya, sehemu mbalimbali wanagundua haya mambo yanaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia tunaona katika uchukuaji wa sheria katika eneo hili kuna upungufu mkubwa sana. Katika eneo hili tunazo kesi 9,538. Kwa masikitiko makubwa nasema, kesi 16 tu ndiyo zimechukuliwa hatua, na hizo kesi siyo kwamba zimemaliza, yaani nne tu ndiyo zimemalizika kwa Serikali kushinda, nne tu walipata haki yao wakaruhusiwa lakini nne ziko katika hatua za usikilizwaji, tatu ziko katika hatua za kutajwa na moja iko katika hatua ya kusubiri hukumu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini cha kusikitisha kesi 1,158 ni za mwaka ulioisha 2023. Sasa tunaenda wapi? Tunawekeza fedha nyingi kwa kuhakikisha tunaandaa utaratibu wa Serikali kuchukua hatua dhidi ya madawa ya kulevya lakini sasa pale wanapogundulika waliofanya hivyo hawapewi haki yao au sheria hazichukuliwi. Kwa kweli ukiangalia kesi 938 na 16 tu ndio zimechukuliwa hatua. Tuna jambo la kujiuliza kama Serikali, tuna jambo la kujiuliza kama Bunge. Tuna jambo la kuhakikisha kwamba tunaisimamia Serikali inahakikisha kwamba wenzetu ambao wanasimamia kesi hizi, haya mashauri; tushauri kitu ambacho kitaisaidia Serikali kuchukua hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa nakuja na ushauri, maana yake ukiziacha kesi hizi, kwanza zinapunguza imani katika mfumo wa haki; lakini pili, ukiangalia kesi hizi kukaa namna hii maana yake tunaendeleza biashara haramu ya madawa ya kulevya. Pia, ukiangalia katika kesi hizi kukaa hivi maana yake jitihada za kupambana na dawa za kulevya zote kwa kweli zinakatishwa tamaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa hiyo hata watumishi wetu …

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, … ambao wanatakiwa kufanya kazi vizuri maana yake watashindwa kufanya kazi kwa wakati…

TAARIFA

MWENYEKITI: Mheshimiwa Florent kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ester Bulaya.

MHE. ESTER A. BULAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpa taarifa mchangiaji mzuri kwa mchango wake na mbali tu hizo jitihada za upambanaji wa dawa za kulevya kushindwa kuungwa mkono kwa watuhumiwa kuchukuliwa hatua stahiki, sasa hivi wamebuni mbinu mpya ya kwenda kuwauzia kemikali bashirifu kwenye zile center za wale warahibu wa drugs. Mwisho wa siku wanatoka kunywa dawa anarudi tena kutumia kemikali bashirifu ambazo ndio mbaya zaidi, nilikuwa naomba nimpe taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Florent, taarifa unaipokea?

MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa naipokea, ina msingi wa kujenga na kuonyesha lazima tuongeze mbinu za mapambano ili kukabiliana na madawa ya kulevya. Mimi naomba kama ambavyo Kamati tumeshauri, tunaomba Bunge liazimie kuanzisha division maalum ya kushughulikia mashauri ya madawa ya kulevya. Tumeona katika maeneo ambapo division hizi zimeanzishwa kazi kubwa imeendelea kufanyika kupunguza haya mashauri ambayo yako pembeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaona division maalum ya ardhi ambayo iliundwa kwa ajili ya kupambana na mrundikano wa kesi za ardhi inaendelea kufanya kazi vizuri lakini tunaona division ya kazi na yenyewe inaendelea kufanya tu vizuri. Kwa hiyo, niombe Bunge lako Tukufu tuanzishe division maalum ya kushughulikia mashauri ya dawa za kulevya kusaidia Taifa letu, kusaidia Mheshimiwa Rais wetu ambaye anataka utawala bora, anataka haki na nchi yetu iweze kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho katika eneo hili naomba nichangie katika Ofisi ya Makamu wa Rais, eneo la muungano na eneo hili naomba nitoe pongezi za dhati kwa Serikali ya Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan na wasaidizi wake, Mheshimiwa Selemani Jafo, Naibu Waziri wake, Katibu Mkuu. Pia, katika eneo hilo tulikuwa na Hoja za Kamati ambayo ilitakiwa hoja za Muungano 25 ambazo zilikuwepo lakini tunaona asilimia 88 za hoja hizo zote zimejibiwa. Maana yake hoja 22 zote zimejibiwa, tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia azimio la pili ilikuwa ni kuhakikisha kwamba taasisi zote za kimuungano zinakuwa na ofisi katika pande zote mbili na tunaona utekelezaji wake hapa ni asilimia 97. Maana yake taasisi 33 zote zina ofisi katika maeneo yote mawili ya muungano na taasisi chache zilizobaki tatu ambazo ni TIC, NBS na TEA na zenyewe ziko katika hatua za mwisho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna kila sababu ya kumpongeza Mheshimiwa Dkt. Samia kwa utayari wake wa utawala bora, kwa uongozi wake wa kufuati haki lakini na utii wa sheria; na tunaamini tukiendelea kumuunga mkono na haya yote basi yatatimizwa. Basi tunaiona Tanzania njema ya kesho na leo; na watu wote wataendelea kuishi kwa ustawi wa utii wa sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nikushukuru kwa muda wako na naunga mkono hoja ya Kamati na naomba Wabunge wote tuungane kwa ajili ya kuunga mkono hoja za Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria, ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Tume ya Mipango wa Mwaka 2023.
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi na mimi kuwa miongoni mwa wachangiaji wa miswada hii ambayo ni ya muhimu sana kwa nchi yetu. Na mimi kama Mjumbe wa Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria nikushukuru pia kwa kutuamini sisi wajumbe wa Kamati ambao kwa kweli tumepitia miswada hiyo kwa uweledi mkubwa kwa kujitoa kwa muda na kuweza kufikia hatua hii ambayo tuko siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mimi nimpongeze sana mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utayari wake kuona mahitaji ya Nchi sasa yanahitaji hii miswada iletwe hapa tuijadili na mwisho wa siku tuipitishe kama sheria kwa ajili ya kutoa huduma kwa ajili ya nchi yetu. Niwapongeze wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, Kaka yangu, Mheshimiwa Boniphace Simbachawene, Naibu Waziri Ridhiwani Kikwete, Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro na Naibu wake Mheshimiwa Pauline Gekul na viongozi watendaji wakiongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi na Makatibu Wakuu na watumishi wote wa hizi Wizara zote mbili. Imekuwa ni kujibizana kwa hoja na mwisho wa siku tunaelekea katika eneo zuri la kuhitimisha miswada hii ikiwa na maslahi mapana ya Nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niongelee kwenye Tume ya Mipango. Tunaona utari ya Mheshimiwa Rais kuja na tume ambayo itafanya kazi kwa uweledi wa mipango ya nchi yetu. Tunajua kwamba utaratibu huu umekuja ukiwa umetathimini pia na kuangalia ni sehemu gani ambapo tulikuwa na mapungufu. Tulikuwa na Wizara ya Fedha na Mipango tukaona kweli nchi inafanya kazi nzuri sana kwenye upande wa fedha, lakini ni nchi gani itaendelea kupiga hatua kubwa kukusanya fedha zaidi isipokuwa na mipango ambayo ni mizuri? Sasa ukiangalia muswada huu wa Tume ya Mipango hiyo yote inakuwa addressed mule ndani inajibiwa. Kwamba tukienda na utaratibu wa muswada huu ukawa sheria basi hayo mapungufu yote ambayo yalikuwa yako katika maeneo ya mipango yatakuwa yamejibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia muundo kwanza ulivyokuja, tukiangalia muundo, na nilikua namsikilia Mheshimiwa Wakili Msomi hapa Dada yangu na Shemeji yangu Makamba, hivi ni kiongozi ambaye ana utayari kujiweka mstari wa mbele, ili mumtathimi kwa kufanikiwa? Hili sasa amelifanya Mheshimiwa Rais kwa yeye kwa Mwenyekiti wa Tume ya Mipango ili tumuone kwamba ana uzalendo na utayari wa kufanya kazi ili aweze kuvusha Taifa letu ambapo yeye ndiye mwenye maono kwa sasa. Kwa hiyo naomba tuondoe shaka kwamba Rais yuko tayari kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo kwa sababu anajua dhamira ya dhati aliyonayo ni kuongoza nchi yetu na kuhakikisha kwamba Tume ya Mipango sasa imekuwa ya uweledi ni yenye mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Wajumbe na Wabunge wenzangu tuondoe shaka kwa Rais kuwa Mwenyekiti wa Tume hii. Lakini tunaona katika eneo hili weledi wa wajumbe wa kamati hawa ambao Mheshimiwa Rais atakuwa anafanya nao kazi; tunaona kwamba ni wakati gani ambao watatumia watu ambao ni wabobezi, watu ambao ni wazoefu katika mipango ili sasa mipango hii ikija ina kuja na mipango ambayo kwa kweli inaakisi taswira ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niendelee kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, sisi tumepitia kwa kina kwa niaba yenu kuhakikisha kwamba Tume hii itakapokuja inakuwa ni tume ya weledi. Mheshimiwa Askofu hapa bishop na yeye alikuwa na wasi wasi kidogo kwamba mipango hii inawezekana isilindwe vizuri mwisho wa siku ikawa ambayo haijalindwa. Lakini Kamati yako tuliliona na tukakaa na Serikali kwenye uboreshaji wa amendmet. Ukiangalia kwamba Ibara 67 (4) kama alivyooma Dada yangu, Mheshimiwa Dkt. Alice, Mpango wowote wa muda mfupi na muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa sheria hii au sheria nyingine iliyotungwa na Bunge na kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara 63 (3) (c) ya Katiba hautabadilishwa na kuachwa kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge. Kwa hiyo, tunaona katika kila nyanja kila sehemu mpango huu umelindwa. Kwa hiyo niwaondoe shaka Waheshimiwa Wabunge kwamba tupo katika mikono salama kuhakikisha mpango huu unafanya kazi na kuwa na maono ambayo imepangwa katika utaratibu ulio mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona wajibu ambao umepangiwa katika tume hii lakini sisi wenyewe ni wahanga na ni mashuhuda wa kuona mipango ikipangwa, utekelezaji unapokuja kufanyika ni kama inakinzana. Leo inakuja TANROADS au TARURA inachimba barabara nzuri kwa rasilimali za nchi, kesho inakuja RUWASA inapitisha bomba inachimba Barabara. Kesho inakuja kuziba kwa rasilimali zile zile za nchi. Lakini kama mipango ilikuwa ni madhubuti inajua miaka mitano ijayo hapa itapita barabara, itapita miundombinu ya maji, utapita Mkongo wa Taifa. Provisons zote zinakuwa zimewekwa, hautaona kwamba tunarudia kutumia rasilimali ya nchi katika kitu kile kile. Kwa hiyo sasa tunakuja na jibu ambalo litakuwa kwa kweli linasaidia nchi yetu kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona katika eneo hili Serikali imekuja na uwazi na kuonyesha kwamba ilipokuwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kweli kuna mambo makubwa ambayo mengine yaliachwa. Tulijikita katika kukusanya fedha na ndio maana nchi yetu inaendelea kupata bajeti lakini kwenye suala la mipango halikufanyiwa katika weledi ule ule ambao inatakiwa. Sasa jibu lake ni nini, ni hili ambalo tupo nalo leo mezani. Waheshimwia Wabunge waamini kwamba baada ya hii sheria kupitishwa tunaamini mipango itakuwa mizuri na ni fedha zipi zinazopatikana bila kuwa na mipango mzuri? Tukiwa na mipango mizuri basi tutapata fedha nzuri na inawezekana tukapata na fedha zaidi. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wajumbe kwamba tumepitia kwa umoja na kujibizana kwa hoja na Serikali suala hili liko kwenye mikono ambayo ni salama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie kwa uchache katika eneo la Sheria ya Usalama wa Taifa. Tuna maboresho mazuri ambayo yamefanyika na tunaona Rais wetu katika sheria hii ina mtambua kama ni Rais ambaye ni msimamizi wa usalama wa Taifa letu, ambaye yeye amepewa ridhaa na wananchi wote wa Tanzania kuhakikisha kwamba nchi yetu iko salama. Kwa hiyo, jukumu hili anapolibeba yeye linakuwa katika hali ambayo tunaamini kwamba tutakuwa wananchi wote tupo katika mikono salama. Lakini tunaona Mheshimiwa Waziri anabaki pale akiwa anasimamia Sera na Bajeti. Kwa hiyo, mahitaji yote ya nchi yatakayokuja katika eneo hilo Waheshimiwa Wabunge watakuja hapa watapitisha, tutajadiliana vizuri, tutafikia muafaka na taasisi zetu zitaendelea vizuri katika kufanya kazi katika uweledi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeona hii Sheria ya Usalama wa Taifa imekuja ikiwa na uwiano unaolingana. Imeangalia maafisa wetu wanavyotekeleza kazi katika mazingira yao kwa unyeti wa kazi yao ikawawekea mazingira ya kufanya kazi lakini ikaangalia pia na haki zao za msingi katika kazi zao wanazozitekeleza. Unapokuwa unatekeleza majukumu kwa bahati mbaya ikatokea bahati mbaya hutakiwi kuhukumiwa kwa bahati mbaya iliyotokea. Ndicho tunachokisema kwamba pasiposhaka huyo mtumishi hatahukumiwa kwa kile kitu alichokitekeleza akiwa katika majukumu yake. Kwa hiyo hayo yote tumeangalia kwa upana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kwamba, na sisi Waheshimiwa Wabunge tujiridhishe kwamba wanaosimamia taasisi hii na wenyewe ni Watanzania ni weledi, wamekula viapo wanapenda nchi yao. Kwa hiyo, hakuna mtumishi anaweza akafanya kitu ambacho ni kinyume na taratibu, ukaona Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa anam-support au Mheshimiwa Rais anam-support, hapana. Kwa hiyo tuamini kwamba kuna watu ambao wapo pale juu yao ambao na wenyewe wanasimamia chombo hiki ili kiweze kufanya kazi kwa weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo yote yameguswa na sisi kama Kamati tumeangalia pia na misingi ya Katiba inafuatwa katika kutunga hii sheria. Tumeona kuna maeneo mengine ambapo kiongozi mkuu wa taasisi hii baada ya kumaliza muda wake ilikuwa inaonekana kwamba huu mtu sasa asipewe majukumu yoyote, ni kama una mfungia. Kufanya jukumu kama hili si adhabu. Kwa hiyo tuliamini kwamba akifanya kazi yake vizuri basi imefika muda kazi yake imemalizika anaweza akapangiwa majukumu mengine. Kwa hiyo utaratibu wa Nchi ambapo itaona inafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi bado niendelee kusisitiza mambo mengi mazuri yameongelewa, naomba Waheshimiwa Wabunge wote tuungane kwa pamoja kupitisha miswada hii yote mitatu kama ilivyowasilishwa kwa maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi, ahsante sana.
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Yatokanayo na Urekebu wa Sheria wa Mwaka 2023 .
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa nafasi na mimi kuwa miongoni mwa wachangiaji wa miswada hii ambayo ni ya muhimu sana kwa nchi yetu. Na mimi kama Mjumbe wa Kamati ya Utawala, Katiba na Sheria nikushukuru pia kwa kutuamini sisi wajumbe wa Kamati ambao kwa kweli tumepitia miswada hiyo kwa uweledi mkubwa kwa kujitoa kwa muda na kuweza kufikia hatua hii ambayo tuko siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mimi nimpongeze sana mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa utayari wake kuona mahitaji ya Nchi sasa yanahitaji hii miswada iletwe hapa tuijadili na mwisho wa siku tuipitishe kama sheria kwa ajili ya kutoa huduma kwa ajili ya nchi yetu. Niwapongeze wasaidizi wa Mheshimiwa Rais, Kaka yangu, Mheshimiwa Boniphace Simbachawene, Naibu Waziri Ridhiwani Kikwete, Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria Dkt. Damas Ndumbaro na Naibu wake Mheshimiwa Pauline Gekul na viongozi watendaji wakiongozwa na Katibu Mkuu Kiongozi na Makatibu Wakuu na watumishi wote wa hizi Wizara zote mbili. Imekuwa ni kujibizana kwa hoja na mwisho wa siku tunaelekea katika eneo zuri la kuhitimisha miswada hii ikiwa na maslahi mapana ya Nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi niongelee kwenye Tume ya Mipango. Tunaona utari ya Mheshimiwa Rais kuja na tume ambayo itafanya kazi kwa uweledi wa mipango ya nchi yetu. Tunajua kwamba utaratibu huu umekuja ukiwa umetathimini pia na kuangalia ni sehemu gani ambapo tulikuwa na mapungufu. Tulikuwa na Wizara ya Fedha na Mipango tukaona kweli nchi inafanya kazi nzuri sana kwenye upande wa fedha, lakini ni nchi gani itaendelea kupiga hatua kubwa kukusanya fedha zaidi isipokuwa na mipango ambayo ni mizuri? Sasa ukiangalia muswada huu wa Tume ya Mipango hiyo yote inakuwa addressed mule ndani inajibiwa. Kwamba tukienda na utaratibu wa muswada huu ukawa sheria basi hayo mapungufu yote ambayo yalikuwa yako katika maeneo ya mipango yatakuwa yamejibiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia muundo kwanza ulivyokuja, tukiangalia muundo, na nilikua namsikilia Mheshimiwa Wakili Msomi hapa Dada yangu na Shemeji yangu Makamba, hivi ni kiongozi ambaye ana utayari kujiweka mstari wa mbele, ili mumtathimi kwa kufanikiwa? Hili sasa amelifanya Mheshimiwa Rais kwa yeye kwa Mwenyekiti wa Tume ya Mipango ili tumuone kwamba ana uzalendo na utayari wa kufanya kazi ili aweze kuvusha Taifa letu ambapo yeye ndiye mwenye maono kwa sasa. Kwa hiyo naomba tuondoe shaka kwamba Rais yuko tayari kuwa Mwenyekiti wa Tume hiyo kwa sababu anajua dhamira ya dhati aliyonayo ni kuongoza nchi yetu na kuhakikisha kwamba Tume ya Mipango sasa imekuwa ya uweledi ni yenye mafanikio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe Wajumbe na Wabunge wenzangu tuondoe shaka kwa Rais kuwa Mwenyekiti wa Tume hii. Lakini tunaona katika eneo hili weledi wa wajumbe wa kamati hawa ambao Mheshimiwa Rais atakuwa anafanya nao kazi; tunaona kwamba ni wakati gani ambao watatumia watu ambao ni wabobezi, watu ambao ni wazoefu katika mipango ili sasa mipango hii ikija ina kuja na mipango ambayo kwa kweli inaakisi taswira ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niendelee kuwaomba Waheshimiwa Wabunge, sisi tumepitia kwa kina kwa niaba yenu kuhakikisha kwamba Tume hii itakapokuja inakuwa ni tume ya weledi. Mheshimiwa Askofu hapa bishop na yeye alikuwa na wasi wasi kidogo kwamba mipango hii inawezekana isilindwe vizuri mwisho wa siku ikawa ambayo haijalindwa. Lakini Kamati yako tuliliona na tukakaa na Serikali kwenye uboreshaji wa amendmet. Ukiangalia kwamba Ibara 67 (4) kama alivyooma Dada yangu, Mheshimiwa Dkt. Alice, Mpango wowote wa muda mfupi na muda mrefu ulioandaliwa kwa mujibu wa sheria hii au sheria nyingine iliyotungwa na Bunge na kuidhinishwa na Bunge kwa mujibu wa Ibara 63 (3) (c) ya Katiba hautabadilishwa na kuachwa kutekelezwa katika muda uliopangwa kutekelezwa bila idhini ya Bunge. Kwa hiyo, tunaona katika kila nyanja kila sehemu mpango huu umelindwa. Kwa hiyo niwaondoe shaka Waheshimiwa Wabunge kwamba tupo katika mikono salama kuhakikisha mpango huu unafanya kazi na kuwa na maono ambayo imepangwa katika utaratibu ulio mzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona wajibu ambao umepangiwa katika tume hii lakini sisi wenyewe ni wahanga na ni mashuhuda wa kuona mipango ikipangwa, utekelezaji unapokuja kufanyika ni kama inakinzana. Leo inakuja TANROADS au TARURA inachimba barabara nzuri kwa rasilimali za nchi, kesho inakuja RUWASA inapitisha bomba inachimba Barabara. Kesho inakuja kuziba kwa rasilimali zile zile za nchi. Lakini kama mipango ilikuwa ni madhubuti inajua miaka mitano ijayo hapa itapita barabara, itapita miundombinu ya maji, utapita Mkongo wa Taifa. Provisons zote zinakuwa zimewekwa, hautaona kwamba tunarudia kutumia rasilimali ya nchi katika kitu kile kile. Kwa hiyo sasa tunakuja na jibu ambalo litakuwa kwa kweli linasaidia nchi yetu kusonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeona katika eneo hili Serikali imekuja na uwazi na kuonyesha kwamba ilipokuwa Wizara ya Fedha na Mipango kwa kweli kuna mambo makubwa ambayo mengine yaliachwa. Tulijikita katika kukusanya fedha na ndio maana nchi yetu inaendelea kupata bajeti lakini kwenye suala la mipango halikufanyiwa katika weledi ule ule ambao inatakiwa. Sasa jibu lake ni nini, ni hili ambalo tupo nalo leo mezani. Waheshimwia Wabunge waamini kwamba baada ya hii sheria kupitishwa tunaamini mipango itakuwa mizuri na ni fedha zipi zinazopatikana bila kuwa na mipango mzuri? Tukiwa na mipango mizuri basi tutapata fedha nzuri na inawezekana tukapata na fedha zaidi. Kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wajumbe kwamba tumepitia kwa umoja na kujibizana kwa hoja na Serikali suala hili liko kwenye mikono ambayo ni salama zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nichangie kwa uchache katika eneo la Sheria ya Usalama wa Taifa. Tuna maboresho mazuri ambayo yamefanyika na tunaona Rais wetu katika sheria hii ina mtambua kama ni Rais ambaye ni msimamizi wa usalama wa Taifa letu, ambaye yeye amepewa ridhaa na wananchi wote wa Tanzania kuhakikisha kwamba nchi yetu iko salama. Kwa hiyo, jukumu hili anapolibeba yeye linakuwa katika hali ambayo tunaamini kwamba tutakuwa wananchi wote tupo katika mikono salama. Lakini tunaona Mheshimiwa Waziri anabaki pale akiwa anasimamia Sera na Bajeti. Kwa hiyo, mahitaji yote ya nchi yatakayokuja katika eneo hilo Waheshimiwa Wabunge watakuja hapa watapitisha, tutajadiliana vizuri, tutafikia muafaka na taasisi zetu zitaendelea vizuri katika kufanya kazi katika uweledi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tumeona hii Sheria ya Usalama wa Taifa imekuja ikiwa na uwiano unaolingana. Imeangalia maafisa wetu wanavyotekeleza kazi katika mazingira yao kwa unyeti wa kazi yao ikawawekea mazingira ya kufanya kazi lakini ikaangalia pia na haki zao za msingi katika kazi zao wanazozitekeleza. Unapokuwa unatekeleza majukumu kwa bahati mbaya ikatokea bahati mbaya hutakiwi kuhukumiwa kwa bahati mbaya iliyotokea. Ndicho tunachokisema kwamba pasiposhaka huyo mtumishi hatahukumiwa kwa kile kitu alichokitekeleza akiwa katika majukumu yake. Kwa hiyo hayo yote tumeangalia kwa upana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kwamba, na sisi Waheshimiwa Wabunge tujiridhishe kwamba wanaosimamia taasisi hii na wenyewe ni Watanzania ni weledi, wamekula viapo wanapenda nchi yao. Kwa hiyo, hakuna mtumishi anaweza akafanya kitu ambacho ni kinyume na taratibu, ukaona Mkurugenzi Mkuu wa Usalama wa Taifa anam-support au Mheshimiwa Rais anam-support, hapana. Kwa hiyo tuamini kwamba kuna watu ambao wapo pale juu yao ambao na wenyewe wanasimamia chombo hiki ili kiweze kufanya kazi kwa weledi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maeneo yote yameguswa na sisi kama Kamati tumeangalia pia na misingi ya Katiba inafuatwa katika kutunga hii sheria. Tumeona kuna maeneo mengine ambapo kiongozi mkuu wa taasisi hii baada ya kumaliza muda wake ilikuwa inaonekana kwamba huu mtu sasa asipewe majukumu yoyote, ni kama una mfungia. Kufanya jukumu kama hili si adhabu. Kwa hiyo tuliamini kwamba akifanya kazi yake vizuri basi imefika muda kazi yake imemalizika anaweza akapangiwa majukumu mengine. Kwa hiyo utaratibu wa Nchi ambapo itaona inafaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi bado niendelee kusisitiza mambo mengi mazuri yameongelewa, naomba Waheshimiwa Wabunge wote tuungane kwa pamoja kupitisha miswada hii yote mitatu kama ilivyowasilishwa kwa maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi, ahsante sana.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi ili niweze kuchangia katika mapendekezo ya bajeti ambayo yamewasilishwa kwetu kwa nafasi ya pekee nikushukuru kwa nafasi lakini pia nimshukuru Rais wetu, Mama yetu mpendwa, Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kwa kuja na bajeti yake ya kwanza ya Awamu ya Sita ambayo kwa kweli inalenga kabisa katika dhima ambayo ni kujenga uchumi shindani na viwanda kwa maendeleo ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, salamu hizi za pongezi zimfikie Rais, lakini ziwafikikie wasaidizi wake askari wake wa miavuli ambaye ni Waziri wetu wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Mwigulu Nchemba Madelu, lakini pia na msaidizi wake Mheshimiwa Masauni Masauni na watendaji wengine wa Serikali bila kusahau michango ya Waheshimiwa Wabunge, Kamati ya Bajeti ambayo inaweza kuboresha mpaka bajeti yao inakuja imesheheni maono mazuri kwa ajili ya wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepitia katika maeneo mbalimbali, nikaona kwamba bajeti yetu hii inaakisi na imeweza kugusa katika makundi mbalimbali ya wananchi ndani ya nchi yetu na hakuna kundi lilobaki. Tumeona katika maeneo ya watumishi ni maeneo mengi ambayo yameguswa kwa ajili ya kuhakikisha sasa watumishi wanakuwa na ari ya kazi kwa kuweza kutenga fedha kwa ajili ya kuwapandisha vyeo, zaidi ya bilioni 449 zinatengwa katika bajeti hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe sisi wote tuunge mkono Serikali kwa kuzipitisha kwa kishindo. Pia tunaona, PAYE, kodi ya mshahara wa mtumishi inapunguzwa kutoka 9% kwenda 8%. Ni mambo mengi mazuri kwa watumishi ambaye tumeona katika Jeshi letu la Polisi, muda wa kuajiriwa katika mkataba wa kudumu unapunguzwa kutoka miaka 12 kuja miaka sita. Tunaona Watendaji wa Vijiji wakipewa posho na Maafisa Tarafa Sh.100,000 kila mwezi. haya ni mambo ya kumshukuru Rais wetu mpendwa, lakini na maono mazuri ya wasaidizi wake, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango kwa kuja na mambo mazuri ambayo yanagusa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, katika eneo hilo tumeona kundi la wanasiasa nalo limeguswa kwa kuona kwamba wawakilishi wa wananchi ambao ni Waheshimiwa Madiwani, na wenyewe posho zao zitoke Mfuko Mkuu wa Serikali Hazina. Mtu ambaye hawezi kuelewa umuhimu wa suala hilo, mimi katika wakati wangu wa maisha niliwahi kutumika kama Mkurugenzi. Nilipoenda kwenye Halmashauri hiyo, nilikuta Waheshimiwa Madiwani hawajawahi kulipwa posho zao kwa miezi 12. Kwa hiyo, ilikuwa ni changamoto kubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naona Serikali imekuja na njia Madhubuti ya kuweza kutatua tatizo hili ambalo lilikuwa la muda mrefu, kuhakikisha Madiwani wetu wanalipwa kwa wakati. Kwa hiyo, niendelee kumpongeza Rais wetu, Waziri pamoja na Naibu Waziri na watendaji wengine ambao wamewezesha hili suala kufanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa ajili ya vijana wetu. Vijana hawa tunawawezesha kupitia asilimia nne za Halmashauri; tunawapa mikopo wananunua bodaboda na wengine wanaajiriwa na wenye bodaboda. Kwa siku moja, kijana wetu anayeendesha bodaboda kipato chake ni shilingi 7,000 mpaka shilingi 10,000. Akikutana na faini ya shilingi 30,000 aidha bodaboda hii anaitelekeza au anaiacha hapo kwa siku nne anakimbia kazi. Kwa hiyo, kwa shilingi 10,000 hata akikopa, maana yake anajua ndani ya siku mbili anaweza kurudisha hizo fedha. Tuendelee kumshukuru Mheshimiwa Rais na Wizara kwa michango mizuri ya namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwa kundi la wananchi ambalo Serikali imeliona hasa kwa kuangalia yale maeneo mahususi kwenye maeneo ya maji, barabara, afya na Bima ya Afya kwa Wote pamoja na uboreshaji wa elimu. Katika eneo hili tunaona tunakwenda kuchanga shilingi mia moja, mia moja katika kila lita ya dizeli na petroli. Ni suala ambalo ni zuri. Naiomba Serikali iendelee kulisimamia ili sasa wenzetu wanaomiliki vyombo vya usafiri wasije wakaona ni sababu ya kupandisha gharama za usafirishaji. Kwa hiyo, Serikali iweze kutoa bei elekezi za nauli na gharama za usafirishaji ili isije ikawa ni mzigo tena kwa wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili, tunaona tozo ya shilingi 10 mpaka shilingi 10,000 kwa muamala wa fedha wa kutuma na kutoa, lakini tozo ya shilingi 10 hadi shilingi 200 kwa laini ya simu ambayo tutaweka fedha; eneo hili niseme, Waheshimiwa Wabunge huku sisi wote ni mashahidi. Wote katika eneo hili tunakubali kuchangia kwa kuwa kila Mbunge hapa leo anaweka na kutoa fedha. Kwa nature ya wateja wetu tulionao, kwa siku wanapiga simu nyingi kulingana na wateja wetu tulionao katika majimbo yetu, lakini kila Mbunge hapa yuko tayari kutoa hizo fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba tuwasihi na wananchi wetu wapendwa, suala hili ni zuri. Tunachoomba sasa Serikali iendelee kusimamia vizuri katika eneo hili, barabara zijengwe, maji yafike kwa wananchi, umeme ufike, lakini pia na bima kwa afya kwa wote iweze kufika kwa wananchi wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Afya
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuweza kuchangia katika bajeti yetu ya Wizara ya Afya. Niungane na wachangiaji wengine kumpongeza Mheshimiwa Rais, Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri anayoifanya kuhakikisha maendeleo ndani ya nchi yetu yanasonga mbele. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kimahsusi nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa mabadiliko makubwa anayoyafanya ndani ya Wizara ya Afya na mahsusi zaidi ndani ya Taasisi yetu ya MSD tulishauri hapa Bungeni na kupitia Wizara yetu chini ya Mheshimiwa Ummy Mwalimu na msaidizi wake Dkt Mollel na wasaidizi wao na Mheshimiwa Rais akaitikia wito akabadilisha uongozi ndani ya taasisi yetu ya MSD na kuweka viongozi ambao ni wataaluma wa dawa, naamini tukiboresha mazingira ndani ya taasisi hiyo tutaona mabadiliko makubwa.

Mheshimiwa Spika, pamoja na mageuzi hayo ya kiutawala lakini bado niendelee kuiomba Serikali. Viongozi hao tumewaweka katika kazi mahsusi. Tusipoweka mazingira ambayo ni wezeshi mazingira ambayo ni rafiki inawezekana tukawakwamisha sisi wenyewe.

Mheshimiwa Spika, sasa niombe, katika eneo hilo la MSD zipo changamoto mbalimbali ambazo tunahitaji kuzifanyia kazi; zingine ni za kikanuni, na zingine ni za kisheria. Mimi nimuombe Mheshimiwa Waziri kwa sababu ni msikivu na ni mtenda kazi anayeamini katika taaluma, hivyo uwape nafasi uliowateua kukusaidia kazi waweze kuleta yale mahitaji na muyafanyie kazi yaweze kufanyika na dawa ziweze kufika katika vituo vyetu na wananchi wapate dawa.

Mheshimiwa Spika, katika eneo hilo kwa uchache tunaona kwamba kazi ya clearance ya dawa kwa Sheria ni kweli imepewa GPSA, lakini bidhaa za dawa vifaa tiba na vitendanishi ni bidhaa ambazo ziko sensitive sana. Unakuta katika process ya manunuzi kuanzia kununua mpaka kusafirisha mpaka kuzi-clear pale bandarini hata ule muda wa matumizi unakuwa umepungua. Hatimaye hizi bidhaa zinaingia mtaani zikienda kusambazwa kwa walaji muda wa matumizi unakuwa umekaribia kuisha. Kwa hiyo saidia, najua ni sheria zipo na GPSA wanafanyakazi kwa mujibu wa sheria lakini bado Bunge Tukufu linaweza likafanya mabadiliko kwa ajili ya kuboresha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika eneo lingine ningependa kutoa mchango wangu mdogo katika jukumu la udhibiti wa chakula na vipodozi. Mwaka 2019 suala la chakula na vipodozi lilihamishwa kutoka Wizara ya Afya likapelekwa katika Wizara ya Uwekezaji Viwanda na Biashara chini ya TBS. Katika utaratibu wa kidunia tukiangalia basic practice duniani kote kwa kweli kidogo katika eneo hilo mpaka leo Tanzania bado watatushangaa.

Mheshimiwa Spika, naomba nichukue historia kidogo. Tukiangalia kuanzia mwaka 1946 tulikuwa na sheria ya The Food and Brad Ordnance Cap. 93. Hii tangu tunatawaliwa na wakoloni mpaka Mwalimu Nyerere mwenyewe alivyokuja hizi bidhaa zilikuwa zinadhibitiwa chini ya Wizara ya Afya. Ilipofika mwaka 1978 Serikali ikaona iboreshe kwa kutenganisha bidhaa hizi kwa kutunga sheria zingine mbili. Ikatunga sheria ya kwanza ya The Pharmacy and Poison Act. ya Mwaka 1978, ikatunga The Food Control Quality ya mwaka 1978. Nia ilikuwa ni kuboresha bidhaa hizi kwa sababu zina linda afya ni kwa ajili ya manufaa ya wananchi wetu. Na Serikali katika taasisi hizi chini ya sheria hizi ikawezesha miundombinu na wataalamu, kazi zikaanza kufanyika.

Mheshimiwa Spika, lakini kwa mabadiliko ya kidunia ilipofika mwaka 2003 kuangalia na mwenendo wa dunia nzima Serikali ikaamua kuziunganisha tena bidhaa hizi na kuvunja sheria hizo mbili na kuunda sheria moja; Sheria ya Chakula Dawa na Vipodozi na Vifaa Tiba Na. 1 ya Mwaka 2003. Katika eneo hili taasisi ambazo zilipewa dhamana ya kusimamia hivi chini ya Wizara ya Afya zimefanya kazi kubwa. Serikali imewekeza fedha nyingi sana katika eneo hili. Imeweka miundombinu ya kutosha mpaka nchi yetu ikapata vigezo vya kimataifa mpaka tukawa na maabara inayotambulika kimataifa tukapata WHO pre-qualified laboratory ambayo unaweza ukapima bidhaa zote ndani ya nchi na nje ya nchi. Haikuishia hapa, tukapata ithibati kutoka WHO ambayo ilikuwa inaonyesha kwamba mifumo ya udhibiti imehakikiwa na inakidhi vigezo vya kimataifa

Mheshimiwa Spika, mwaka 2019, kama nilivyotangulia kusema, mabadiliko yakafanyika; inawezekana yalikuwa na nia njema. Hata hivyo, hata hivyo bidhaa hizi zikaenda kurushwa sehemu ambayo ukiangalia kwenye Blue Print ya Taifa letu si majukumu yake. Kwa hiyo kupelekwa TBS ambayo yenyewe inadhibiti viwango na ukaipelekea udhibiti tunaenda kuhatarisha afya ya wananchi.

Mheshimiwa Spika, ukiangalia bidhaa hizo madhara yake ni makubwa sana, na taarifa za takwimu za WHO ukiangalia katika dunia nzima magonjwa zaidi ya 200 yanatokana na ulaji wa vyakula ambavyo si salama. Lakini ukiangalia watu milioni 600 katika uwiano wa mtu mmoja katika watu 10 wote hao wanapata madhara wanapokula vyakula ambavyo si salama. Lakini tukiangalia watu 420,000 hufa kila mwaka kwa kula vyakula ambavyo si salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tukiangalia fedha zinazotumika duniani dola za kimarekani bilioni 110 zinatumika katika kutibu magonjwa yanayotokana na vyakula hivyo.

Mheshimiwa Spika, sasa mimi niombe sana katika eneo hili. Serikali inakuwa inafanyakazi nzuri kuhakikisha kwamba itapata matokeo mazuri lakini katika eneo hili matokeo siyo mazuri na mimi nishauri na nimshukuru Mwenyezi Mungu kwamba Mheshimiwa Ummy Mwalimu, nafikiri Mwenyezi Mungu ana makusudi yake. Wakati suala hili linafanyika najua ulipambana sana kulizuia katika Wizara yako, na kipindi hicho nilikuwa sijajua kama nitakuwa Mbunge; lakini halikufanikiwa na leo Mwenyezi Mungu amekurudisha humo humo katika Wizara hiyo hiyo na leo sasa na mimi naliongelea.

Mheshimiwa Spika Mheshimiwa Waziri na msaidizi wako suala hili; na inawezekana kwa kiasi kikubwa mlishaanza kuifanyia kazi. Okoa maisha ya Watanzania.

Mheshimiwa Spika, vipodozi hivi vinaleta kansa ambazo nimesikia Waheshimiwa Wabunge wanasema. Hakuna mchawi, ni kwamba sisi tumeamua kuweka vipodozi watu watumie wanavyotaka. Unalala asubuhi unakuta mtu shape iko hivi, baada ya muda mfupi madhara yake ni yeye na hospitali, hospitali na yeye; kwa hiyo hatuwezi kusema kwamba tunatafuta mchawi ilhali hapa tumeongelea saratani na hivyo vipodozi ambavyo havijadhibitiwa vimekaa mtaani. Sisi tuna uchungu na wananchi, na Bunge lako Tukufu limepewa dhamana hii kushauri Serikali kuhakikisha kwamba inafanyia kazi maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini tunaona matatizo ya figo pamoja na matatizo ya ini yataendelea kuongezeka. Nasimama hapa, nasema, tukiangalia miaka miwili ijayo mbele inawezekana tukawa na madhara ya magonjwa mengi kwa ajili ya kuziacha hizi bidhaa mtaani zikiwa hazina udhibiti na zikiachiwa taasisi ambayo si jukumu lake. Kwa hiyo niombe sana niombe sasa Mheshimiwa Waziri kupitia Wizara yetu ya Afya basi ifanye utaratibu mapema ili bidhaa hizi ziende katika eneo linalokubalika, ambalo ni Wizara ya Afya chini ya mamlaka ya Chakula na Dawa na vipodozi au yoyote itakavyoitwa….(Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini nimalizie kusema…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Kengele ya pili imeshagonga Mheshimiwa, ahsante sana.

MHE. FLORENT L. KYOMBO: …nikushukuru, naunga mkono hoja, ahsante sana, nashukuru sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nishukuru kwa nafasi. Naomba niungane na wenzangu kumpongeza sana Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi nzuri inayofanyika katika majimbo yetu lakini na Taifa letu kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, wana-Misenyi wamehemewa kwa mambo mazuri ambayo yamefanyika ndani ya miaka miwili ambayo nitayataja kama sehemu ya pongezi kwa wana-Misenyi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hatuwezi kumpongeza Mheshimiwa Rais bila kuwapongeza pia wasaidizi wake; na nikianza na Waziri wetu wa Ofisi ya Rais TAMISEMI, Naibu Waziri ndugu yetu Ndejembi na Daktari kwa kumsaidia Waziri kufanya kazi nzuri. Niseme dada yetu Mheshimiwa Waziri umeanza vizuri; na kwa mikutano ambayo unatuunganisha katika mikoa kabla ya kuja kwenye bajeti ukaona mapungufu yanayohitajika ni sehemu ambayo umeupiga mwingi na Mwenyezi Mungu aendelee kukuongoza katika hilo.

Mheshimiwa Spika, Pamoja na Wizara kufanya vizuri lakini katika ngazi za Mikoa tumeona viongozi wetu ndani ya mikoa wanafanya kazi nzuri ya usimamizi; na hivyo nichukue fursa hii kumpongeza sana Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa wa Kagera Albert Chalamila na RAS wake Pamoja na viongozi wote. Niseme ndugu yangu Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa tunakuelewa wana Kagera piga kazi na endelea kutusimamia katika Mkoa wetu. Lakini pia na uongozi wa Wilaya ya Misenyi, nikitambua Mkuu wangu wa Wilaya, Madiwani wote, Mkurugenzi pamoja na watumishi, wote tunafanya kazi kwa umoja na ushikamano ndio maana mambo yanaonekana ndani ya kipindi cha miaka miwili.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa tunaongea lugha nyingine ndani ya Wilaya ya Missenyi. Tunayo Hospitali mpya ndani ya miaka miwili, tuna vituo vya afya vipya viwili na pia zipo zahanati za kutosha na Serikali bado mnaendelea kutuletea fedha ambazo tunaendelea kujenga majengo mengine. Lakini leo tunasimama ndani ya miaka miwili tuna shule ya sekondari mpya, madarasa 53 mmetuletea na leo Mheshimiwa Waziri tumepokea barua kupitia Mradi wa BOOST tunaenda kujenga shule ya Msingi mpya na madarasa mengine 20; ni pongezi nyingi kwa Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya pongezi hizo sasa wana- Misenyi bado wanayo mahitaji mengi kwa nia njema kwa sababu wameshaonjeshwa maendeleo mazuri wanapenda maendeleo sasa yaendelee kufika mpaka ngazi za vitongoji.

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Misenyi, kama ambavyo alitangulia kusema kaka yangu Mheshimiwa Jasson Rweikiza Mkoa wa Kagera kwa ujumla tuna mvua takribani asilimia 80 ya muda wote wa mwaka. Nimeona Mheshimiwa Waziri umekuja na utaratibu mpya, bei elekezi hizi za ujenzi wa madarasa mabweni na vyoo; hii model uliokuja nayo tuombe uipeleke pia na kwenye upande wa ujenzi wa barabara. Ukitoa bajeti linganifu katika mikoa yote na majimbo yote kwa sehemu ambazo tunapata mvua kubwa hiyo bajeti inakuwa haitoshi. Wana-Missenyi wanatambua kuwa miaka miwili nyuma tulikuwa tunapata milioni 700 lakini leo tunapata bilioni 2.4, ni ongezeko kubwa sana, lakini bado uhitaji ni mkubwa.

Mheshimiwa Spika, na kwa kuwa miundombinu imeendelea kujengwa mpaka katika maeneo ya vitongoji mahitaji ya barabara yameongezeka; na sisi Wilaya ya Misenyi tumeleta maombi ya kuongeza mtandao wa barabara kilomita 131.7. ninachoomba naomba Mheshimiwa Waziri aipokee na reflection ya bajeti ya Wilaya ya Misenyi kwa mwaka huu katika kilomita zetu tulizokuwa nazo 921.7 basi mwaka huu 131.7 iongezeke tuwe na mtandao wa kilometa 1,053 ili tuweze kufika kule amabako Mhehsimiwa Rais amepeleka shule, amepeleka zahanati na amepeleka vituo vya afya. Niombe sana katika hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini lingine, mwaka juzi tulijengewa barabara ya lami ambayo ilikuwa ni ahadi ya Mheshimiwa Rais aliyeko madarakani. Kutoka Hospitali Teule ya Mgana tukajenga kilometa 1.2, kipande kilichobaki ni kilometa 4.6. Hatupendi kulalamika Mheshimiwa Rais akija kwetu najua ipo ndani ya uwezo wa Mheshimiwa Waziri. Mwaka huu tuongezewe bajeti tuendeleee na kilomita angalau mbili ili angalau mwaka unaokuja angalau tuweze kumaliza barabara hiyo na wananchi waweze kuona ahadi njema Mheshimiwa Rais inaweza kutekelezwa kwa wakati. Najua hilo Mheshimiwa Waziri analiweza.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kwenye upande wa afya ambapo wana-Misenyi wanamshukuru Mheshimiwa Rais, tunavyo vituo vya afya vipya viwili; lakini issue ni vifaa tiba. Wilaya ya Misenyi hatujapata vifaa tiba kabisa; lakini pia suala la watumishi, kama wenzangu walivyoongea, tuombe sasa tuweze kuongezewa watumishi ili wananchi waweze kupata huduma inayotakiwa. Pia kwenye mpango unaokuja, zipo kata za kimkakati ambapo tukipata vituo vya afya katika Kata za Buzinga, Buyango, Kitoga, Bugandika, Kilemile, Mabale, Mtukura na Minzilo angalau kwa Wilaya ya Misenyi kwa coverage iliyopo ya huduma za afya utakuwa ume cover vizuri na wananchi wataendelea kushukuru. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine ni ombi la wana-Misenyi. Pamoja na kushukuru kwa shule mpya ambayo tumeletewa, na madarasa ya msingi manne nimeshapeleka ombi kwa Mheshimiwa kwako ka kushirikiana na uongozi wa Wizara yangu kupitia Katibu Tawala wa Mkoa. Kuna mabadiliko kidogo naomba ayabariki, yatakuwa yana-reflect hali halisi na uhalisia kwenye ground kule. Kwa hiyo hili nitakuwasilishia nitaomba ulibariki ili tuweze kwenda vizuri na wananchi waendelee kushukuru kwa kazi nzuri ya Mheshimiwa Rais.

Mheshimiwa Spika, lingine niende kuomba kwa upande wa…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. FLORENT L. KYOMBO: …naona umewasha king’amuzi; basi nikushukuru, naomba kuunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa nafasi ya kuchangia katika Wizara yetu ya Maji. Niungane na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nzuri ambayo inafanyika ndani ya Wilaya ya Misenyi, Jimbo la Nkenge na hasa kwa huduma ya maji ambayo tukiangalia historia ya miaka miwili iliyopita na sasa, tuko sehemu nzuri sana kwa miradi iliyotekelezwa.

Mheshimiwa Spika, niwapongeze sana Waziri Mheshimiwa Aweso, Naibu Waziri Mheshimiwa Maryprisca Mahundi, kwa kazi nzuri wanayoifanya, lakini nyuma yao wapo watu ambao wanawapa support. Kwa nafasi ya pekee pia, nimpongeze dada yangu Katibu Mkuu, Nadhifa Kemikimba, lakini na Ndugu yetu Bwana Cyprian Luhemeja, ambao na wenyewe wanashiriki kwa kiasi kikubwa kuhakikisha kwamba, wanasogea.

Mheshimiwa Spika, Wizara inafanya kazi nzuri, lakini na katika mikoa yetu wapo watendaji ndani ya Wizara hii ambao wanafanya kazi vizuri. Nichukue fursa hii pia kumpongeza Regional Manager wa Mkoa wa Kagera, ndugu yangu Warioba Sanya. Pia na Meneja wangu wa Wilaya ya Misenyi, bwana Andrew Kiembe, pamoja na timu zao zote kwa sababu, wanafanya kazi kwa ushirika. Mheshimiwa Waziri kama anavyojua anao watoto wengi, lakini anao wa BUWASA. Ninaye ndugu yangu pale John Silati naye, Mtendaji Mkuu wa BUWASA pamoja na wasaidizi wake wanafanya kazi nzuri, wanamwakilisha vizuri Mheshimiwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kabla sijachangia nimpongeze Mheshimiwa Waziri, kulikuwa kuna mfumo ambao kidogo ulikuwa unachelewesha utendaji kazi wa manunuzi wa kikanda, sasa hivi ameupiga chini, ameuweka ngazi ya Mkoa. Nimpongeze sana kwa sababu ni hatua kubwa ambayo inarahisisha kazi kwa wasaidizi wake na kazi ikaenda kwa speed kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasimama hapa nikiwa nina furaha kubwa kwa niaba ya wananchi wa Misenyi. Kazi imefanyika kubwa, kata 20 zote leo tunapoongea nyingine tumemaliza suala la maji katika kata nzima, lakini sehemu nyingine tuko katika mkakati wa kupeleka maji pale. Tukiangalia Kata ya Gera maji yameenda katika vijiji vyote wananchi wanapata maji safi na salama. Ukiangalia Kata ya Ishozi mradi mkubwa wa maji uko pale, sasa hivi maji yanawekwa kwenye tenki ili ku-test mifumo, ili kuona maji sehemu ambapo yanaenda vizuri na sehemu ya kurekebisha.

Mheshimiwa Spika, pia tukiangalia Kata ya Buyangu, Serikali imetuletea fedha, mradi umekamilika, wananchi wa Rutunga, wananchi wa Rwamachi wanapata maji na eneo la Buyangu lililobaki tunaona tunapata maji kutoka mradi mkubwa wa Kata ya Kitobo ambapo vijiji vitano vyote vya Kata ya Kitobo, lakini na huku Vijiji vya Kishoju, Rushasha na Kikono watapata maji kutoka kwenye mradi huo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaona Kata ya Nsunga mradi umekamilika na Kijiji cha pembeni cha Ngando sasa hivi kisima kinachimbwa ili kiweze kupelekewa maji. Nimwombe Mheshimiwa Waziri ambacho, wakandarasi wetu pale katika maeneo hayo miradi hii wakati mwingine malipo yanachelewa. Jana ametuambia mahususi kwamba, pochi la mama limefunguka, tuombe basi wakandarasi hawa wapate fedha zao kulingana na maombi yao na kazi waliyofanya ili sasa waweze kukamilisha hizo kazi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunao Mradi mkubwa wa Kyaka - Bunazi. Mheshimiwa Waziri mradi huu ni mkubwa sana na amefanya juhudi yeye pamoja na Wizara yake kuhakikisha kwamba unakamilika na ulikamilika. Mheshimiwa Rais amekuja ameuzindua mwaka jana, lakini kuna kazi kubwa ambayo wameifanya kwa kutumia akili ya kuhakikisha wanavusha maji kutoka upande wa Kyaka kwenda upande wa Kasambya kupitia katikati ya Mto Kagera. Ilisumbua sana kitaaluma kupitisha chini ya daraja, ikaonekana sio kweli, lakini wamezama ndani ya maji, maji yakavuka, lakini mwuombe Mheshimiwa Waziri thamani ya kuvusha maji yale kule mbele kwa wananchi bado haijaonekana vizuri kwa sababu, bado kuna maeneo ambayo wananchi hawajapata maji.

Mheshimiwa Spika, tukiangalia katika Kijiji cha Gablanga maji hayajafika, lakini ukiangalia Kakindo maji hayapo. Ukiangalia Mabuye sehemu imepata maji, lakini sehemu nyingine maji bado hayajafika, lakini pia ukiangalia Nyabiyanga maji yamepita baadhi ya maeneo. Tungependa kwamba, Mheshimiwa Waziri akipeleka maji katika Kijiji fulani, vitongoji vyake vyote amemaliza na hiyo kazi inakuwa imeisha.

Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Kyaka tunaona katika Vitongoji vya Nyakashaga, Doga, lakini pia na Bungabo bado maji hayajafika. Kwa hiyo, nimwombe Waziri kwa kazi kubwa iliyofanyika katika eneo hilo, basi aweze kukamilisha mradi huo ili uweze kuwa mradi wenye thamani kwa wananchi ambao wako katika Makao Makuu ya Wilaya ya Misenyi.

Mheshimiwa Spika, niipongeze Serikali, wakati naingia hapa kilio changu kilikuwa ni kuhakikisha kwamba, tunapata maji kutoka Ziwa Victoria na Mheshimiwa Waziri ninaposema Ziwa Victoria sisi kwetu ni hatua kumi kwenda ziwani, sio kama hizi kilometa nyingine ambazo zinaombwa kwa sababu, Ziwa Victoria liko hapo kandokando ya kata zetu. Sasa kilio changu ni Kata ya Kashenye, Mradi kutoka Ziwa Victoria sasa hivi ni mwaka wa pili, lakini nimshukuru Mheshimiwa Waziri, nimewasiliana na wataalam wangu kwamba, sasa hivi Mradi mkubwa wa Maji kutoka Ziwa Victoria kwenda katika Kata ya Kashenye katika Vijiji vyote vya Kashenye, Bukwali na Bushago, sasa hivi unaanza na taratibu za manunuzi zimeshafanyika.

Mheshimiwa Spika, mradi huu hauishii Kashenye unaenda mpaka Kata ya Kanyigo yote ili watu wapate maji safi na salama ya uhakika, unaenda Kata ya Bwanja. Nimwombe Mheshimiwa Waziri kuna kata jirani za pale ambazo zina shida ya upatikanaji wa vyanzo vya maji, kwa mfano, nikisema Kata ya Bugandika; nimwombe mradi huo ukishakuja kwa phase hizo jinsi walivyojipanga kibajeti, basi hata hizo kata ambazo ziko jirani zina shida ya kupata vyanzo tuziangalie ili mradi huo sasa uweze ku-extend mpaka Kata ya Bugandika ili wananchi waweze kupata maji safi na salama. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naangalia maeneo mengine ambayo sasa katika bajeti ya 2023/2024 tumeweka kwenye bajeti, Kata ya Bugorora hakuna maji, lakini tunaona Kata ya Minziro. Niombe Mheshimiwa Waziri fedha hizo kinapofika kipindi cha bajeti basi tupate fedha hizo ili wananchi hawa wa kata hizo na wenyewe wasijione wapweke kwa sababu, katika kata nyingine kama nilivyosema miradi ya maji kwa kweli, ni mizuri, ni ya uhakika na mingine inaendelea. Ni pongezi sana kwa Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna kata nyingine ambazo zinahitaji maboresho, bado tunatafuta vyanzo vya maji. Kata ya Ruzinga bado mpaka sasa hivi suala la maji halijawa la uhakika, lakini tunaona Kata ya Ishunju, Mabali na Kirimilile na eneo la Mutukula, niombe sana. Tumeomba fedha milioni 450 Mheshimiwa Waziri ni kidogo kwa Kata ya Mutukula kupeleka maji katika vitongoji vyake ambavyo ni vitatu, ambavyo havina maji.

Mheshimiwa Spika, kwa kusema maneno hayo, nikushukuru kwa nafasi. Naamini sasa bajeti ya Misenyi itakamilika ili wananchi waweze kupata maji. Ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. FLORENT L. KYOMBO: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa nafasi. Kwa nafasi ya pekee nishukuru Serikali yetu kupitia Wizara yetu ya Fedha kwa Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba pamoja na wasaidizi wake kwanza kwa kuleta mpaendekezo ya maeneo gani ambayo Serikali inaweza kukusanya fedha na tukaweza kuzipata kwa ajili ya shughuli mbalimbali za maendeleo katika nchi yetu. Hiyo tunaiona kwa kuthibitisha kupitia huu Muswada wa Fedha ambao utasaidia utekelezaji sasa wa hayo maeneo ambayo ni mapya katika ukusanyaji wa fedha hizo uweze kufanyika kwa urahisi lakini pia kufanyika kwa mujibu wa sheria za nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo machache tu katika maeneo machache pia ni ushauri ili kuendelea kuboresha ili utekelezaji wa maeneo haya uweze kusaidia kwenda vizuri lakini pia na kuweza kupunguza matumizi mengine ambayo yanaweza yakawa ni makubwa zaidi kuliko ambavyo tungeweza kushauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo la Sheria ya Local Government kwenye eneo ambalo sehemu ya 9 ambayo imeonesha marekebisho mbalimbali lakini pia kuna suala la ushuru wa sehemu za maegesho kupitia TARURA ambayo imekuwa ni chanzo kizuri cha fedha kwa ajili ya kuongeza fedha hizo kwa ajili ya kuchangia ujenzi wa barabara zetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hilo naunga mkoo hoja mapendekezo yote ambayo Serikali imekuja nayo lakini kuna maboresho jinsi ya utekelezaji wa sehemu hiyo ambayo kimsingi naamini Serikali hii ni moja inafanya kazi moja. Nikiangalia kwa undani TARURA ni taasisi ambayo imeanzishwa muda si mrefu kwa hiyo hata manpower (Resource) ya watu iliyonayo na baadhi ya section katika Taasisi hiyo bado inakuwa ni changa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, kuna maeneo mengine ambayo nakuwa naona kwa kuwa Serikali ilishaweka miundombinu hasa katika Local Government kuanzia katika ngazi ya wilaya mpaka ngazi ya kitongoji ambazo zote mfumo uko vizuri katika usimamizi.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mchango wangu katika eneo hili nilikuwa nashauri fedha hii ya maegesho ni kweli iendelee kuwa ni fedha ambayo inakusanywa kwa ajili ya TARURA lakini means ya kukusanya zile fedha ningeshauri Halmashauri ingekusanya hizo fedha kwa niaba ya TARURA na hizi fedha sasa zikaelekezwa kwa mfumo mzuri wa kisheria zikawa zinapelekwa kwa ajili ya kufanya kazi hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme ni kwa sababu gani? Kwa sababu, kitu cha kwanza halmashauri inazo posi ambapo posi hizo zinatumika kukusanya mapato yote na katika posi hiyo unaweza ukaweka provision nyingi za ukusanyaji wa mapato hata kama yakiwa ni mapato zaidi ya 1,000. Lakini halmashauri hizo hizo zinazo manpower mpaka ngazi za mitaa, ngazi za vitongoji na vijiji.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia katika wilaya zetu structure ya wilaya, tuachane na zile wilaya ambazo ziko katika miji mikubwa labda manispaa. Halmashauri zingine za wilaya zina visehemu vidogo vidogo vinavyokua kimji kwa hiyo unakuta TARURA yenyewe huwa inawezekana kukusanya maegesho katika eneo la Mji Mkuu lakini huku ambako ni mji mdogo ambao umechangamka na parking zipo za magari unakuta maeneo hayo ukusanyaji unakuwa ni mgumu kwa sababu gani, kwa sababu TARURA haina watu wa kutosha kusimamia katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia, hata TARURA ikijielekeza ku-out source kwamba imeingia na kampuni gharama ya usimamizi au kuilipa ile kampuni kukusanya zile hela ndogo zinazopatikana katika maeneo ambayo ni pembezoni mwa miji ni kubwa kuliko hata makusanyo yenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu wa pili ni kuipongeza Serikali hasa kwa upande wa ukusanyaji wa Property Tax ambapo katika mchango wangu wa awali nilisema ilikuwa ni eneo lililoshindikana. Nimshukuru Mheshimiwa Waziri kuja na mawazo mazuri na njia iliyotumika ni nzuri na sahihi. Nimeshukuru kuona katika kifungu hiki imeongezwa kwamba asilimia 15 ya fedha hizi zitarudishwa katika Wizara husika ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa kama gawio la Halmashauri.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo hili ni zuri kwa sababu tunajua haya maeneo yako ndani ya halmashauri zetu lakini halmashauri lazima iendelee kutenga na kuboresha makazi ya wananchi wetu. Kwa hiyo, kurudisha hii fedha itasaidia sasa Halmashauri kuendelea kufanya kazi ambayo ilikusudiwa. Pamoja na kukusanya Property Tax lakini basi tuendelee kuboresha maeneo hayo ili sasa wananchi wetu waone kile wanachokichangia, fedha inapoenda Serikalini inarudi na kuendelea kuboresha maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo langu la mwisho nataka kushauri, kwenye Bill hapa sijaiona vizuri, lakini niombe kama ambavyo wamefanya katika Property Tax kwenye asilimia 15 na hili suala la wajasiriamali ambao wanatumia vitambulisho tuliangalie. Wajasiriamali wetu wanafanya kazi katika magulio na katika masoko na katika hotuba ya bajeti ya Mheshimiwa Waziri tunaenda kuwapa vitambulisho ambavyo vinawasaidia kwa kweli, wanalipa Sh.20,000/= wanakuwa hawasumbuliwi, lakini ni jinsi gani halmashauri inaenda kuboresha yale maeneo ambayo wajasiriamali wetu wanafanyia biashara zao?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naomba kama ambavyo tumefanya kwenye Property Tax tunaweza tukaona namna gani gawio kidogo linalotokana na makusanyo ya vitambulisho vya wajasiriamali likarudi tena kule halmashauri ili basi waendelee kuimarisha magulio na masoko ili sasa wananchi wetu wafanye kazi au biashara zao katika mazingira ambayo ni rafiki. Iwekwe miundombinu ya vyoo na maji na huduma nyingine za kijamii zinazotakiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili nilitaka kuchangia hayo machache. Nakushukuru kwa nafasi na naunga mkono Muswada wetu uweze kupita kwa kishindo. (Makofi)