Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Dr. Pius Stephen Chaya (27 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nami nachukua nafasi hii nikushukuru wewe, lakini kipekee sana namshukuru Mwenyezi Mungu na nimshukuru sana Rais wetu Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kazi kubwa ambayo ameifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wote ni mashahidi kwamba wakati Mheshimiwa Dkt. Magufuli anaingia, nchi yetu ilikuwa inakusanya mapato machache sana. Hivi sasa tuna uwezo wa kukusanya zaidi ya shilingi trilioni mbili kwa mwezi. Haya ni mafanikio makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya maombi yetu yote ambayo tunayatoa hapa ya maji, elimu na barabara hayawezi kutokea iwapo hatutamuunga mkono Rais katika kusimamia ukusanyaji wa mapato. Kwa hiyo, nawaomba Wabunge wenzangu, tutakapofika Bunge la Bajeti, tuweke mikakati ya kuisaidia Serikali ili tuwezekuongeza mapato, ili haya mahitaji ya Watanzania ambayo wote tuna azma kubwa ya kuitimiliza, yaweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja ya Rais, lakini pia nampongeza kwa kuja na approach ya kuanzisha Mamlaka ya Maji yaani RUWASA. Sisi sote ni mashahidi, kabla hatujaanzisha Wakala wa RUWASA, maji na upatikanaji wa maji katika vijiji vyetu ilikuwa shida sana.

Mheshimiwa Spika, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki, tuna mradi mmoja mkubwa wa shilingi bilioni 11 wa Kitinku/Lusilile. Huu mradi una-cover vijiji 11 na tayari tumeshapata takribani shilingi bilioni mbili. Mbali ya kwamba tumeanzisha hizi Wakala, bado nina ushauri kwa Wizara ya Maji. Ushauri wa kwanza ni kwamba nadhani tusiwe na utitiri wa miradi ya maji. Tujitathmini kwa miradi ambayo tumeianzisha, tutengeneze acceleration plan, kwamba kwa kipindi gani tutamalizia ile miradi ambayo tayari tumeshaianzisha.

Mheshimiwa Spika, Rais wetu ni mtu wa matokeo, anataka kuona matokeo kwa kitu alichokianzisha. Kwa hiyo, naishauri sana Wizara ya Maji, kwa miradi ambayo tumeianzisha, tusikimbilie kuanzisha mradi mpya, tutengeneze acceleration plan ya lini tutamalizia ile miradi, halafu tuangalie ni jinsi gani tunaweza ku-scale up hii approach ambayo tumeanza nayo kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba Wizara ya Maji iongeze wigo wa financing ya Mfuko wa Maji. Kutegemea chanzo kimoja ku-finance miradi ya maji, bado naona tunaipa mzigo sana Serikali. Naomba wakati Bunge la Bajeti likifika Wabunge tuangalie jinsi gani tutaisaidia Wizara ya Maji, tuje na options mbalimbali za kupanua wigo wa kuongeza financing mechanism ya miradi ya maji.

Mheshimiwa Spika, suala la TARURA, vilevile namuunga mkono Rais hasa kwa kuanzisha Wakala wa Barabara (TARURA). Sote ni mashahidi, kulikuwa na tatizo kubwa sana la ujenzi wa barabara za TARURA, lakini wachangiaji wengi wameelezea suala la kuongeza na kubadilisha allocation formula ya 70 kwa 30.

Mheshimiwa Spika, nina hoja mbili; hoja ya kwanza, nadhani tatizo ni ile fixed approach, kwa sababu tunatumia 70 kama ilivyo na 30 kama ilivyo. Nashauri tuwe flexible. Mahitaji ya utengenezaji wa barabara yanategemeana na demand ya mwaka huo. Kuna kipindi demand ya barabara ya vijijini ni kubwa kuliko demand ya barabara za mjini ambazo zinasimamiwa na TANROADS. Nashauri sasa kwamba inapofika kipindi ambacho tunahitaji kupeleka bajeti TARURA na TANROADS, basi mfuko wa barabara usikilize mawazo ya TARURA na TANROADS, wa-present waone kwamba je, kweli TARURA wanahitaji asilimia 30 au wanahitaji zaidi ya asilimia 30? Hiyo ndiyo hoja yangu.

Mheshimiwa Spika, lingine nashauri kwamba, tuna- depend sana kwenye chanzo kimoja cha ku-finance TARURA. Tuna-depend sana kwenye fuel levy, ambacho nadhani kimelemewa. Nashauri Bunge lako tukufu tutafute options nyingine za ku-finance TARURA. Badala ya kusema tuongeze asilimia 30, nadhani kuna haja sasa ya kuhakikisha tunaongeza wigo.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Chaya.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana na naunga mkono hoja ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nachukua nafasi hii nikushukuru sana kwa nafasi uliyonipatia. Pia nimshukuru sana Dkt. Mwigulu pamoja na timu yake kwa kuja na huu Mpango mzuri sana. Mapendekezo yangu yatajikita kwenye usimamizi wa miradi ya kimkakati. Wewe mwenyewe unatambua kwamba tumefanya mambo makubwa sana katika nchi hii katika miradi ya kimkakati ukiwepo ununuzi wa ndege zaidi ya 10, ujenzi wa reli ya kisasa, lakini vile vile tunategemea kuanza ujenzi wa bandari mbalimbali hapa Tanzania.

Mheshimiwa Spika, hapa Dodoma tumekuwa na miradi ya kimkakati mingi sana. Hivi karibuni wenzetu wa Jiji la Dodoma wamemaliza ujenzi wa hoteli kubwa sana ambayo itakuwa five star haya yote ni maendeleo makubwa sana ambayo yameletwa na Serikali ya Chama Cha Mapinduzi. Sasa hoja yangu ni kwamba, katika hii miradi ya kimkakati ambayo ni uwekezaji mzuri sana kwa nchi yetu, lakini nalitazama katika upande wa usimamizi. Kwa sabbau tayari tuna sera ya Public Private Partnership, Sera ya Ubia kati ya Serikali pamoja na wadau mbalimbali wa maendeleo hususan Private Sector, lakini tuna sheria ya ubia kati ya Public Sector and Private Sector. Nadhani ni muda muafaka sasa sisi kama Serikali tuangalie jinsi gani tunaenda ku-capitalize kwenye hii sera ili tuweze kuisadia Serikali.

Mheshimiwa Spika, nataka kushauri kwa mfano, tuna mradi mkubwa hapa Dodoma wa hoteli, hoteli ya five star, je, tunaenda kutumia business modal gani kuhakikisha kwamba ile hoteli inaenda kufanya kazi vizuri. Kwa nini tusiingie kwenye huu ubia sasa wa Private Sector na Public Sector tukaangalia ni maeneo gani ambayo Private Sector wana uwezo nayo tukawaachia, halafu yale maeneo ambayo sisi tuna uwezo nayo tukayafanyia kazi. Hilo ni la kwanza ningependa kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, lingine, tuna miradi mingine ambayo ni mikubwa tunaifanya. Sasa hivi tunasisitiza suala la Public Private Partnership, naomba nimshauri Waziri kwa nini wasiunde task force ikaenda kupitia miradi yetu yote ile mikubwa wakaja kuishauri Serikali kuja na business modal ya jinsi gani tunaweza ku-manage hii miradi. Kwa nini tusiende kwenye ile management contract kwamba eneo ambalo Serikali tuna uwezo nalo tutalifanyia kazi, lakini yale maeneo ambayo Serikali hatuna uwezo nayo, nashauri tunahitaji kuchukua maamuzi magumu ili kuhakikisha kwamba Private Sector na yenyewe ili iweze kukua tunahitaji kuigawia sehemu ya ile miradi ili waweze kuisimamia. Kuna faida nyingi katika hili.

Mheshimiwa Spika, kwanza, tunaenda kukuza ajira; Pili, tunaenda kukuza mahusiano kati ya Public Sector na Private Sector; na Tatu, itatufanya sisi tulale. Badala ya Waziri wa Fedha kulala anawaza kwamba sijui mradi huu haufanyi vizuri, una-transfer risk, unampelekea mtu mwingine, kazi yetu inabaki kukusanya kodi lakini vile vile kuangalia gawio letu mwisho wa mwezi.

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii, naomba kwamba Serikali ichukue haya maoni yangu na iyafanyie kazi. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa nafasi hii lakini nimshukuru sana Waziri kwa kuleta Mpango huu. Nimeupitia Mpango huu ni mzuri sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nishukuru kwa miradi mikubwa ambayo tumeiwekeza kwa miaka mitano. Huo ndiyo mwelekeo sahihi wa nchi, lazima tuwe na capital investment. Kama tunataka hili Taifa baadaye liwe lenye heshima lazima tuanze kuwekeza sasa hivi kwenye miradi ya muda mrefu; miradi ya umeme, barabara, reli na ununuzi wa ndege. Bila kufanya hivyo litakuwa taifa lenye aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kwenye tatizo la ajira kwa vijana wetu wanaomaliza vyuo vikuu. Watu wengi wameongelea kero mbalimbali upande wa elimu kwamba elimu yetu ni mbovu na kadhalika. Mimi naomba niwatoe mashaka kwamba ingekuwa mbovu mimi leo nisingekuwa Daktari hapa wa Policy, ingekuwa mbovu Mwigulu leo asingekuwa Daktari pale wa Uchumi. Nadhani kuna maeneo ambayo sisi kama wataalam tunahitaji kuishauri Serikali, ni case by case na tusi-generalize. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimepitia Mpango huu kwa kweli naomba niseme tunahitaji kuja na chapter ya pekee ni jinsi gani tunakwenda kutatua tatizo la ajira kwa vijana wetu waliomaliza vyuo vikuu. Mimi naomba nijikite kwa vijana waliomaliza vyuo vikuu tu kwa ngazi ya cheti, diploma na digrii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilikuwa Mwalimu wa Chuo Kikuu cha Dodoma na nimefundisha Chuo cha Mipango, nina vijana wangu ninaowafahamu wamemaliza wana miaka 8 bado wapo mtaani. Wanaoathirika zaidi ni watoto wa maskini ambao hawapo aggressive, hawajui wapi pa kuanzia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashauri nini Serikali? Kwanza, natambua kuna program ndani ya Ofisi ya Waziri Mkuu ambayo inaendeshwa na ndugu zetu wa TAESA, wengi tumepiga kelele hapa kwamba vijana wanamaliza vyuo hawana uwezo, huwezi kupata uwezo chuoni, uwezo tunaupata kwa kupitia on job training. Kule tunafundisha theory lakini lazima tuje na programu ambayo itawahamisha wale vijana kutoka kwenye theory kwenda kwenye practice na ndiyo kitu ambacho Ofisi ya Waziri Mkuu wamefanya kupitia program hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wamefanya nini? Wamechukua vijana kama internship program wamewaweka pale kwa mwaka mmoja wakawapa token ya 150,000 then wakawasaidia kuwa-groom, wanawapitisha kwenye zile life skills, interpersonal skills, communication skills, computer skills na kadhalika, aki-graduate pale wanam-link na job seekers au wale supplier wanaotaka watu kwa ajili ya kuwaajiri. Hiki ndiyo kitu ambacho mimi nashauri huu Mpango ujikite kwamba tuendeleze ile program ambayo imeshaanza, financing yake ambayo bado ipo weak vijana wanapomaliza vyuo wajiunge pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nataka tuje na Sera ya Internship. Tuna vijana wengi wapo mtaani tunalalamika kwenye vituo vya afya hakuna watoa huduma wa afya, tunalalalmika kwenye sekondari hakuna walimu lakini tuna vijana wengi mtaani. Ile program ambayo Waziri alikuja nayo wanawapa shilingi 150,000 kwa mwezi kwa nini tusiifanye hiyo program tuajiri vijana wale tuwaweke kwenye health facilities, tuwalipe shilingi 150,000. Kwanza itakuwa tumewapunguzia stress ya maisha, tumepunguza stress ya wazazi kuwatunza na tumepunguza stress ya watoto wa kike kuolewa tukawaweka pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunahitaji kuja na hiyo program kwenye huu Mpango kwamba sasa internship program iwe compulsory, tutengeneze sera na sheria kijana yeyote akishamaliza ile miaka mitatu anakuwa mainstreamed kwenye internship program. Akishamaliza pale, hapa sasa uhusiano kati ya TAESA na Sekretarieti ya Ajira, nitashangaa kuona Sekretarieti ya Ajira unamuacha kijana ambaye Mheshimiwa Waziri amem-groom mwaka mzima kupitia internship program unaenda kumchukua mtu hajapita kwenye program hiyo. Tunapiga kelele vijana hawana skills, hizo skills tutazijenga kwa kupitia internship program na Sekretarieti ya Ajira sasa fanyeni kazi na TAESA ili kuhakikisha kwamba vijana wanaokuja kule hatutakuwa na malalamiko hawawezi kujieleza, tayari tumeshawa-groom kwa mwaka mmoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine hili ni la Wizara tofauti. Tunapoenda kutumia hii program ya internship, nataka tuje na kitu kinaitwa policy maximum, hebu sisi kama nchi tujiwekee ukomo wa kisera, kijana asikae zaidi ya miaka miwili tangu amemaliza chuo. Tunajisikia aibu vijana wanakaa miaka mitano mtaani wanatembea na vyeti, sisi wenyewe tumewafundisha, tumewekeza na tunataka warudishe zile kodi. Hebu tuje na sera ambayo nimei-propose tuweke kiwango cha ukomo kwamba sasa Viwanda, Uwekezaji na watu wengine ambao sisi ndiyo creators wa kazi tukae pamoja tutengeneze modeling ya vitu gani ambavyo tunahitaji kuvifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kitu kimoja, kwa mfano, kwenye huu Mpango sijaona zile ajira milioni 8 ambazo tumeahidi tunaendaje kuzifikia? Tunahitaji kufanya modeling mwaka wa kwanza tutahitaji kufikia labda watu milioni mbili, mwaka wa pili milioni 3. Halafu pia tunawapataje hawa, ni kutoka private sector au public sector? Hicho kitu natamani kifanywe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni Mfuko wa Kuchochea Ajira kwa Vijana. Nashukuru Mheshimiwa Waziri ameliweka vizuri kwenye Mpango wake na namuunga mkono lakini naomba niboreshe kwenye ….

T A A R I F A

MBUNGE FULANI: Taarifa.

SPIKA: Taarifa, nimekuona Mheshimiwa.

MBUNGE FULANI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mchangiaji kwamba vijana wanaomaliza vyuo vikuu akiona zizi la ng’ombe, akiona kinyesi anakimbia, akiona banda la kuku anakimbia. Vijana hawa wanaomaliza chuo kikuu hawajapata mahali popote pale pakwenda ku- practice hata kama ni kilimo kidogo. Shule zetu kuanzia sekondari tumeondoa mashamba darasa, hakuna mahala ambapo mwanafunzi anaenda ku-practice.

Mheshimiwa Mwenyekiti, graduate anawazungumzia mchangiaji hawajawahi ku-practice hivyo vitu kuanzia wanaanza darasa la kwanza mpaka wanamaliza hiyo degree. Mimi napigiwa simu kama Mbunge, Mheshimiwa Mbunge tunaomba utusaidie kazi, nawauliza kazi gani? Wanasema kazi yoyote hata kufagiafagia. Hii inaonesha kwamba mpaka anamaliza chuo kikuu haja-define exactly na kile kinachofanyika nyumbani kwake ufugaji na kilimo haoni kama ni kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba nimpatie taarifa mwalimu ambaye amefundisha chuo kikuu muda mrefu kwamba watoto kwa upande wa ku-practice vitu ambavyo tunataka viendeleze taifa kwenye kilimo hawa graduates hawajapata fursa hiyo na ni weupe kabisa. Ukimwambia chips kuku anakimbilia kuila ila mchakato wa kupatikana kwa mayai na viazi hataki kusikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante sana. Mheshimiwa Dkt. Chaya muda wako ulishapita, nilikuvumilia tu.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa nafasi. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nachukua nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa hii nafasi. Kipekee namshukuru sana Profesa pamoja na timu yake ya Wizara ya Elimu kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo naenda kujikita kwenye mfumo wa elimu. Nimefanya uchambuzi wa mfumo wa elimu na nimejikita kwenye zaidi ya nchi 15 ambazo nimefanya uchambuzi. Nimepitia mfumo wa elimu wa Tanzania, Japan, America, UK, Kenya, China na vile vile nimepitia mfumo wa elimu wa Zanzibar. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hoja takriban nne ambazo ningependa kuziwasilisha. Baada ya kupitia mifumo yote hii ya elimu, hoja ya kwanza niliyogundua inaleta utofauti kati ya elimu yetu na elimu nyingine duniani ni suala la muda wa kuanza Darasa la Kwanza na pili suala la umri wa kuanza darasa la kwanza. Vile vile ni aina ya elimu ambayo tunaitoa katika ngazi ya vyuo vikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya pili ambayo nimeigundua baada ya kupitia mifumo mbalimbali ya elimu duniani ikiwepo ya Zanzibar na ya Tanzania, kuona ni stage gani ambayo elimu yetu inatakiwa iwe academic, lakini ni stage gani ambayo elimu yetu inatakiwa iwe technical na ni stage gani ambayo tunahitaji kuwa na mixture ya technical na academic? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya tatu ambayo nimepitia nikagundua ni suala la miundo ya mitaala. Katika miundo ya mitaala nimegundua vitu viwili; ya kwanza, ukipitia mitaala yetu kuna tatizo kubwa sana la masaa ya kukaa darasani na vile vile masaa ya kufanya practical, (field work).

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nimeangalia mfumo wa assessment. Katika mfumo huu nilichojifunza, hususan mfumo wetu wa Tanzania, unawaandaa vijana kuwa na exam fear ambayo ni mbaya sana. Katika hili wasiwasi wangu uliopo ni kwamba tumeweka uzito mkubwa sana kwenye mitihani. Unakuta mitihani ya mwisho ina takriban asilimia 70 lakini yale mazoezi ambayo yanaenda kumjengea uwezo yana asilimia 30. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja ya mwisho ni hoja ambayo Waziri wa Elimu alisema kwamba wanakuja na mfumo wa ku-review sera yetu ya elimu ya Taifa, lakini vile vile kupitia mitaala yetu ya Elimu ya Taifa. Hoja yangu ni kwamba wakati Wizara inajipanga kwenda kufanya mapitio ya hii sera, nadhani ni muda muafaka sasa wa kujikita kikamilifu kuhakikisha kwamba tunakuwa na comprehensive review ya sera. Tuwe na muda wa kutosha katika ku-review and then tuje tujikite katika ku-review mitaala. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, maana yangu ni kwamba tunahitaji kuwa na sera ambayo itakuja ku-inform hiyo curriculum ambayo tunaitaka, lakini tunahitaji kuwa na sera ambayo itakuwa customized kulingana na case studies mbalimbali tulizokutana nazo katika nchi mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali baada ya kutoa hoja zangu hizo takriban tano, la kwanza, kama nilivyotangulia kusema, naomba nimshauri Waziri kuwa suala la mapitio ya Sera ya Elimu ni suala la msingi sana. Naomba tunavyopitia Sera ya Elimu ya Taifa, tufanye harmonization na wenzetu wa Zanzibar. Zanzibar elimu ya msingi wanaenda miaka sita, lakini tuna labour mobility ya kutoka Zanzibar kuja Bara, Bara kwenda Zanzibar. Ni muda muafaka sasa tufanye harmonization ya hii mifumo yetu ya elimu ili kuhakikisha kwamba tunapokuwa na wenzetu wa Zanzibar tunaongea lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ilifanyie kazi. Tunahitaji kuwa na mfumo mmoja wa elimu kwa sababu Bara na Zanzibar ni nchi moja, nasi hatuna restrictions zozote kwenye masuala ya elimu. Kwa hiyo, hilo naomba tulifanyie kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, ni suala la kuondoa ile tunaita exam fear. Katika kuondoa exam fear mimi nina hoja ifuatayo: Nimefanya kazi vyuo vikuu. Nimefundisha Chuo Kikuu cha Dodoma muda mrefu na pia nimefundisha Chuo cha Mipango muda mrefu. Kitu nilichojifunza na nimekisema, nadhani kuna tatizo kwenye curriculum zetu. Tumeweka weight kubwa sana kwenye mitihani ya mwisho ambayo inatengeneza exam fear. Mwanafunzi anahangaika ili aweze kupata A na B, badala ahangaike kupata competency. Nataka kushauri kwamba katika hili naomba sasa unapopitia mitaala na sera, punguza weight ya mitihani, peleka weight kwenye practicals, vijana tuwa-expose kwenye mazingira ya kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la nne, naishauri Serikali tuanzishe kitu kinaitwa integrated education system. Tuje na combination ya academic na technical. Wabunge wengi wameelezea. Mheshimiwa Waziri wewe unafahamu, tumesoma huko nyuma kwenye shule ambapo tulikuwa tunafundishwa sayansikimu, elimu ya kilimo na vitu vingine, lakini ile elimu ilikufa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunapotaka kuandaa vijana waweze kujitegemea, ni muda muafaka sasa kuhakikisha kwamba tuna-impart hizi competences kuanzia huko chini shule ya msingi, sekondari na ile inawajengea palatability ya kupenda, kwamba baadaye niende nikasomee mambo ya kilimo, baadaye nikasomee ufundi na kadhalika. Huwezi kujenga palatability ya mtu akiwa level ya juu, unataka aende akasomee ufundi VETA. Tunahitaji ku-instill kuanzia chini shule za msingi na sekondari ili wale vijana anapotoka pale anasema mimi nataka niwe fundi wa bomba.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Kuna taarifa, sijajua inatoka wapi? Mheshimiwa Mwita Getere.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, hapa. Nilitaka nimpe msemaji hapa…

NAIBU SPIKA: Ngoja ngoja. Kulikuwa na taarifa kutoka pale, ndiye niliyemwita. Kwa hiyo, wewe subiri kidogo.

Mheshimiwa Mwita Getere.

T A A R I F A

MHE. BONIPHACE M. GETERE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Nataka kumpa taarifa Mheshimiwa anayeongea kwamba rushwa siyo lazima iwe kwenye pesa peke yake. Corruption of mind ni jambo kubwa sana katika nchi za Kiafrika na hasa Tanzania. Kuna haja gani ya kutomwekea mtoto maarifa ya kufundishwa namna ya kufuga kuku, namna ya kufuga ng’ombe, namna ya kulima, ukamshindilia ma-pai, ma-triangle na mambo mengi ambayo watoto wengi wanaotoka primary siyo kwamba wote wanaenda sekondari, wengi wanabaki vijijini. Wanaobaki vijijini wanabaki na nini?

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwita Getere, tafadhali naomba ukae kidogo. (Kicheko)

Waheshimiwa Wabunge, taarifa tunazozitoa inabidi ziendane na Kanuni zetu. Mbunge anayeruhusiwa kusema kuhusu taarifa ni pale ambapo Mbunge mwenzake halafu kuna jambo anataka kumpa taarifa iliyo sahihi. Pengine kile anachokisema kimekaa namna fulani hivi. Sasa nimeona Wabunge wanasimama kusema taarifa, wakati anataka kuchangia yeye wazo lake. Sasa hiyo ni kinyume na kanuni zetu, ndiyo maana huwa kuna nafasi ya kuchangia. Usiwe na wazo lako unataka kumpa mwenzako ili na yeye alifanye wazo lake, hapana. Unampa taarifa kwenye kile kile anachokizungumza.

Mheshimiwa Dkt. Pius Chaya, taarifa kutoka kwa Mheshimiwa…

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Hamna Taarifa juu ya taarifa. Kwa hiyo, uwe unasubiri kidogo, tutaenda vizuri tu, hamna shida.

Mheshimiwa Dkt. Chaya unapokea taarifa ya Mheshimiwa Getere?

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru. Napokea Taarifa ya Mheshimiwa Mbunge na nadhani alikuwa anaunga mkono hoja na mawazo ambayo nilikuwa nayatoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kingine ambacho ningependa kuishauri Serikali ni upande wa vyuo vikuu.

NAIBU SPIKA: Kuna taarifa nyingine. Sasa kwa utaratibu kwa sababu tunajifunza, akishazungumza mmoja akitoa taarifa, lazima mzungumzaji azungumze ndiyo mwingine anaomba tena taarifa. Kwa hiyo, kwa sasa kwa sababu hilo tulikuwa hatujalielewa vizuri, nitakupa nafasi Mheshimiwa Saashisha, lakini kwa kawaida ukikaa chini namna hiyo, akishasimama kuzungumza akaongea, unaomba upya taarifa.

Mheshimiwa Saashisha.

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ahsante pia kwa mwongozo mzuri. Nataka kumpa msemaji taarifa kwamba hapo awali kabla ya mwaka 1919 Wizara ya Elimu ilikuwa na mfumo rasmi kabisa wa shule za msingi za ufundi na kwetu kule Hai tulikuwa na shule tano zenye muundo huo. Yaani watoto wakiwa shule ya msingi walikuwa wanafundishwa pia masomo ya ufundi na kulikuwa na walimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka ninavyozungumza sasa hivi, shule ya msingi ya ufundi Mshara kuna walimu ambao waliandaliwa kwa ajili ya mitaala hii kufundisha rasmi masomo ya ufundi. Tatizo ni kwamba shule hizi zimeachwa hazijaendelezwa. Kwa hiyo, nampa taarifa kwamba kulikuwa na mfumo huu, ila umelala. (Kicheko/Makofi)

NAIBU SPIKA: Waheshimiwa Wabunge, nawakumbusha kwenye vishkwambi vyenu zimo Kanuni mle. Tuzipitie vizuri. Huko tunakoelekea kwenye hili Bunge ni mwisho mwisho wa kujifunza Kanuni. Baadaye itakuwa ni mtu kaa chini, sogea kidogo, futa ulichosema. Sasa hivi tunaenda taratibu.

Mheshimiwa Dkt. Chaya malizia mchango wako.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakubali vile vile taarifa ya Mheshimiwa Mbunge na bado naendelea kuishauri Serikali kwamba tunahitaji kuhuisha mitaala yetu hususan katika ngazi ya shule za msingi na sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho upande wa vyuo vikuu. Kwa uzoefu wangu ambao nimekaa kwenye vyuo vikuu, unakuta kwa mfano wale wanaosoma certificate, diploma, na degree tuna wa-subject kwenye kufanya research. Mwanafunzi gani wa certificate anaweza kufanya research ikatumika katika maisha yetu? Mwanafunzi gani katika level ya diploma anaweza akafanya research ikatumika katika maisha yetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kushauri, Wizara ya Elimu, mje na mfumo unaoitwa capstone project system; huu mfumo unaweza ukatumika kwa ngazi za chini ambao unawajengea uwezo wale watu, tunawa-expose kwenye mazingira ya kazi, wanakuja na ubunifu, innovations. Unaweza ukamchukua mtu ukampeleka kwa mfano TANESCO, anaenda kubuni mradi fulani na ile inakuwa na weight kubwa kama nilivyotangulia kusema huko. Badala ya kuweka weight kubwa kwenye mitihani tunatengeneza fear of exams. Tupeleke weight kubwa kwenye hizi capstone projects ambazo zitasaidia kuwajengea competences na skills. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, namwomba Waziri, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki sina Chuo cha VETA na nina vijana wengi sana waliomaliza sekondari wanahitaji kuwa na Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nichukue nafasi nikushukuru sana kwa hii nafasi. Vile vile nichukue nafasi hii kipekee kumshukuru sana Waziri wa TAMISEMI, dada yetu Mheshimiwa Ummy pamoja na timu yake kwa kazi nzuri ambayo anaifanya.

Mheshimwa Naibu Spika, tunamfahamu vizuri sana dada yetu Mheshimiwa Ummy, hatuna wasiwasi kabisa na utendaji wake. Pia tunawafahamu Manaibu wake vizuri sana, hatuna wasiwasi kabisa na utendaji wao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina mambo matatu ambayo nahitaji kuishauri Serikali. Jambo la kwanza nitashauri kwa upande wa afya ya msingi, jambo la pili nitashauri upande wa barabara na madaraja na jambo la tatu nitashauri kuhusu suala la ugatuzi wa madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natoka katika Jimbo la Manyoni Mashariki. Jimbo langu la Manyoni Mashariki lina zaidi ya vijiji 60. Katika vijiji vile 60 nina vijiji 29 ambavyo vina Zahanati. Vile vile nina Kata 19 na katika Kata hizo, nina Kata mbili ambazo zimejengewa Vituo vya Afya. Kwanza nachukua nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kutujengea Vituo vya Afya viwilli; Kituo cha Afya cha Kintinku ambacho tayari kimeanza kutumika na Kituo cha Afya cha Nkonko ambacho tayari kilishakamilika, lakini bado kuna changamoto za hapa na pale.

Mheshimiwa Naibu Spika, Kwa hiyo, nachukua nafasi hii kumshukuru sana Waziri, lakini naomba nimkumbushe mambo mawili. Jambo la kwanza, kwenye Vituo vya Afya viwili ambavyo vimejengwa hususan Kituo cha Afya Nkonko tayari kimekamilika, lakini bado hatuna wataalam. Tulipeleka mtaalam mmoja ambaye ni Daktari (Medical Doctor), hakuweza kuripoti. Kile Kituo cha Afya ni kikubwa sana, kinahudumia zaidi ya Kata sita. Naishukuru tena Serikali kwa kutupa hiyo nafasi, lakini bado kile Kituo cha Afya hakitumiki.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba niishauri Serikali, kwa sababu tuna tatizo la hao wataalam kwenda kwenye Vituo vyetu vya Afya, nadhani tunahitaji kuja na mbinu mbadala. Naishauri Serikali husasan Wizara ya TAMISEMI tuangalie jinsi gani tunaweza tukafanya mapping ya wale vijana waliomaliza Shahada za Udaktari kwenye kanda husika, kwa mfano, Kanda ya Kati ili tunapowapangia vile vituo, tupange kulingana na kikanda. Hii itapunguza kasi ya vijana kutowasili au kutoripoti kwenye vituo vyao. Naomba nilishauri hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa nawaza kuhusu balance kwamba, kati ya kujenga Kituo cha Afya na Zahanati kipi kianze? Natambua kwamba Sera yetu ya Afya inatambua kila Kata lazima iwe na Kituo cha Afya, kila Kijiji lazima kiwe na Zahanati, lakini katika Ilani ya Chama cha Mapinduzi vile vile imebaini kwamba kila Kata inatakiwa iwe na Kituo cha Afya, lakini kila Kijiji kiwe na Zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu nini? Ni wakati gani sasa tunahitaji kuanza kujenga Kituo cha Afya na ni wakati ambapo tunahitaji kuanza kujenga Zahanati? Hoja yangu inajikita kwenye eneo langu la Jimbo la Manyoni Mashariki ambapo nina vijiji zaidi ya 60 lakini nina Zahanati 29 tu; nina Kata zaidi ya 19 na Vituo Afya viwili. Nadhani Mheshimiwa Waziri unahitaji kuangalia zaidi jinsi ya ku- balance unapofanya maamuzi aidha uanze ku-exhaust Zahanati kwenye Kata then twende kwenye kujenga Kituo cha Afya, badala ya kujenga Kituo cha Afya kwenye Kata ambayo haina Zahanati.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nalisema hili? Kuna vijijij vipo mbali sana na kupata huduma za afya. Ningetamani kuona kila Kijiji kinapata Zahanati, then ile Kata ambayo tayari ina Zahanati i-qualify kupata Kituo cha Afya. Lengo letu ni kupunguza umbali wa watu kupata huduma za afya, lakini vilevile ku-promote suala health seeking behavior ili watu wasikimbilie kwenye dawa za kienyeji.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili ni suala la barabara. Naishukuru Serikali kwanza kwa Kuanzisha TARURA, nilishasema huko nyuma; na kwa Jimbo la Manyoni Mashariki tuna mtandao wa barabara zaidi ya kilomita 1,000 na bajeti yetu kwa mwaka tunapata takribani milioni 600. Mwaka huu tumekumbwa na matatizo makubwa sana ya kuharibika kwa barabara, barabara ya Kintinku Makanda takribani kilomita 30 imejifunga kuanzia Januari mpaka sasa hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, Makanda kuna mnada mkubwa sana ambao unachangia pato la Wilaya yetu ya Manyoni, lakini tuna barabara ya kutoka Iseke - Mpapa - Simbanguru – Mangori, ilijifunga kwa muda mrefu sana. Vile vile tuna barabara ya kutoka Chikuyu - Chibumagwa - Mahaka kwenda Sanza, nayo ilijifunga kwa muda mrefu sana. Tunahitaji kufanya nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani ni muda muafaka, watu wengi wamesema tunahitaji kuipa nguvu TARURA, naunga mkono hilo. Kwa upande wa Manyoni Mjini ningemshauri Mheshimiwa Waziri hasa kwa mijini, wilaya ambazo tunazo, Makao Makuu ya Wilaya, sidhani kama bado TARURA wanahitaji kuendelea kukarabati kwa kiwango cha vumbi.

Mheshimiwa Naibu Spika, natamani kuona katika bajeti ya Mheshimiwa Waziri wanatenga angalau kilomita moja kwa ajili ya kujenga barabara za mijini, Makao Makuu ya Wilaya kwa kiwango cha lami, kuliko kuja na barabara za vumbi kwenye Makao Makuu ya Wilaya. Hizi barabara za changarawe na vumbi tuzipeleke vijijini, Natamani kuona tunaboresha Makao Mkuu yetu ya Wilaya.

Mheshimiwa Naibu Spika, sanjari na hilo, vile vile natamani kuona mnapokuja na mpango wa kujenga barabara za lami kwenye maeneo ya Makao Makuu ya Wilaya tuangalie jinsi gani tutaweka taa za barabarani kwa ajili ya kuboresha miji yetu na vilevile kuwafanya wafanyabishara weweze kufanya kazi kwa muda mrefu na pia itaboresha usalama wetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la mwisho ni suala la ugatuzi wa madaraka. Mimi ni muumini wa ugatuzi wa madaraka, nimehusika sana katika mchakato wa kuandaa Sera ya Ugatuzi Madaraka. Wote mnatambua kwamba suala la ugatuzi wa madaraka lilianza miaka ya 1998 ambapo tulianza na D by D Policy Paper, ambayo imekaa kwa zaidi ya miaka 20, lakini hatujawahi kuwa na Sera ya Ugatuzi wa Madaraka.

Mheshimiwa Naibu Spika, D by D Policy Paper ndio ilitumika kama sera ambayo tumeitumia sana kuja na program ya kwanza ya maboresho ya Serikali za Mitaa na program ya pili ya maboresho ya Serikali za Mitaa ambayo iliisha 2014. Kuanzia mwaka 2019, natambua TAMISEMI walianza mchakato wa kutengeneza Sera ya Taifa ya Ugatuzi wa Madaraka. Hoja yangu ni nini? Napenda kujua kutoka kwa Mheshimiwa Waziri, mchakato wa ile sera ya ugatuzi wa madaraka imefikia wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, namshukuru Mheshimiwa Waziri, katika bajeti yake ameweza kutenga fedha kwa ajili ya program ya kuimarisha Serikali za Mitaa na Mikoa, yaani Regional and Local Government Strengthening Program. Napenda kujua kwamba ni kwa jinsi gani sasa Wizara inakuja kuwahusisha wadau wa maendeleo?

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba katika kuandaa hii program na hata hii Sera ya Ugatuzi wa Madaraka, wadau mbalimbali walihusika sana wakiwepo USAID, UNICEF, EU, DFID, JICA na wengine: Je, Mheshimiwa Waziri amejipangaje kuhakikisha anawahusisha hao wadau ili kiasi cha one point five billion ambacho tumekipanga kwenye bajeti yetu tuweze kupata nguvu vilevile ya wadau ambao walihusika sana katika kuhakikisha kwamba suala la ugatuzi wa madaraka linaenda kupata kipaumbele?

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya, naomba nichukue nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri na timu yake na ninaomba niseme kwamba naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nachukua nafasi hii kukushukuru sana wewe, nimshukuru kipekee kabisa Waziri, Mheshimiwa Eng. Dkt. Chamuliho na vile vile nawashukuru manaibu wake wawili. Nachukua nafasi hii niwashukuru sana ndugu zangu wa TANROAD Mkoa wa Singida, wamekuwa proactive sana tunapopata matatizo sisi Wilaya ya Manyoni hususan panapotokea matatizo ya kuharibika kwa barabara. Kwa kweli hili naomba niwashukuru sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hoja tatu ambazo zinaendana na ujenzi wa barabara, lakini vile vile nina hoja ambayo itahusiana na suala la ujenzi wa daraja na hoja nyingine ambayo nataka kuchangia inahusu Kituo cha Pamoja cha Ukaguzi wa Magari (One Stop Inspection Station) ambacho kipo katika Jimbo la Manyoni Mashariki.

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi natoka katika Jimbo la Manyoni Mashariki. Kwanza nichukue nafasi hii nimshukuru sana Waziri, katika bajeti hii ambayo ameiwasilisha kuna daraja ambalo linajulikana kama Daraja la Sanza ambalo limekuwepo ndani ya Ilani ya Chama cha Mapinduzi kwa miaka 10. Nafurahi na namshukuru sana Waziri kwa sababu tayari upembuzi yakinifu ulishafanyika, tayari usanifu wa kina ulishafanyika na tayari zaidi ya 90% ya wananchi walishalipwa fidia zao. Namshukuru sana Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sanjari na hilo, kwa mwaka huu wa fedha, Waziri ametutengea takribani shilingi bilioni 1.5 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa hili daraja. Hoja yangu ya msingi, nataka kupata majibu haya wakati Waziri anakuja kuhitimisha kwa sababu hili daraja limekuwa likipangiwa hela kila mwaka lakini haliendi kutekelezeka. Nitapenda kusikia sasa kutoka kwa Waziri: Je, ni lini sasa huo ujenzi wa daraja utaanza? Wamejipangaje kuhakikisha kwamba wanatangaza hizo tenda ili Wakandarasi waanze hiyo kazi ya kujenga daraja? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine nina barabara ambayo Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliiahidi alipokuja wakati wa kuninadi wakati wa kampeni. Barabara ya kutoka Manyoni - Heka - Sanza ambayo inaenda mpaka Chaligongo barabara inaenda mpaka Mbabala - Bihawana inatokea Dodoma. Hii barabara ina umbali wa takriban kilomita 200. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hii barabara ina umuhimu mkubwa sana. Kwanza hii barabara inagusa Halmashauri nne. Inagusa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, inagusa Halmashauri ya Wilaya ya Itigi, inagusa Halmashauri ya Wilaya ya Bahi na Halmashauri ya mji wa Dodoma. Kwa maana nyingine, hii barabara inaunganisha mikoa miwili; Mkoa wa Singida na Mkoa wa Dodoma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kubwa zaidi, hii barabara ni muhimu sana kwa ukuaji wa uchumi wa mikoa miwili hususan Mkoa wa Dodoma na Mkoa wa Singida. Tuna wakulima wengi sana ambao wapo katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki, Jimbo la Bahi na Jimbo la Dodoma Mjini.

Mheshimiwa Naibu Spika, zaidi ya hilo tuna Game Reserve ya Kizigo ambayo ni maalum kwa Utalii wa Uwindaji. Hiki ni kitega uchumi muhimu sana ambapo kwa kweli tunahitaji kuhakikisha hii barabara tunaiimarisha, nini hoja yangu? Ni muda muafaka sasa kwa sababu Rais Hayati John Pombe Joseph Magufuli alituahidi na tayari ipo ndani ya hii bajeti, lakini haijatengewa fedha. Sasa napenda kusikika kutoka kwa Waziri ni lini tunakuja kujipanga kufanya upembuzi yakinifu (feasibility study), lakini tunakuja kuanza kupanga na kuweka bajeti kwa ajili ya detail design na vile vile, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa hii barabara angalau kwa awamu? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu Wabunge wengi wameeleza kilio chao cha barabara mbalimbali, wote tunatambua hizi barabara ambazo zinaunganisha zaidi ya halmashauri mbili, lakini barabara ambazo zinaunganisha mikoa zaidi ya miwili, ni barabara muhimu sana kwa uchumi wa Taifa letu. Kubwa zaidi ndugu zangu wa kutoka kwenye haya majimbo manne wanapata huduma zao nyingi za kiafya Dodoma, hususani katika hospitali ya Mkapa lakini hospitali ya Uhuru na hata Hospitali yetu ya General hapa Dodoma. Kwa hiyo, utaona ni kwa jinsi gani Serikali inahitaji ku-invest kwenye hii barabara ili tuweze kukuza uchumi wa maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ni hiki Kituo cha Pamoja cha Ukaguzi wa Magari ambacho kinajulikana kama One Stop Inspection Station na kipo katika Kijiji cha Muhalala. Hiki kituo kimefikia asilimia 50 ya ujenzi wake yaani execution rate na kwa mwaka huu tumetengewa milioni 120 kwa ajili ya ujenzi wa hiki kituo na tayari pale kuna magofu ya majumba zaidi ya miaka miwili yamekaa mradi ulikuwa umesimama. Hoja yangu ni nini? Kwanza nitapenda kujifunza kutoka kwa Waziri je, hii milioni 120 imewekwa kwa ajili ya vitu gani? Ningependa kupata narrative ya hii milioni 120 inaenda kukamilisha asilimia ngapi? Nasema hivi kwa sababu amesema kwamba ni asilimia 50 tu ambayo tayari tumeshakamilisha, bado asilimia 50. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili ningependa kujifunza kutoka kwa Waziri vilevile, atuambie kwamba, je, anategemea huu mradi utaenda kukamilika lini? kama umekaa miaka miwili Serikali haijapeleka fedha, then mwaka huu anatuwekea milioni 120 na tayari ni asilimia 50 tu ndiyo ambayo imeshakamilika, je, hiyo milioni 120 itaenda kukamilisha hiyo asilimia 50. Kwa hiyo, ningependa kupata majibu haya kutoka kwa Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nirudie tena kumshukuru sana Waziri, lakini vilevile, niwashukuru sana ndugu zangu wa TANROADS Mkoa wa Singida, wamekuwa na mchango mkubwa sana. Tuna barabara yetu ya kutoka Solya kwenda Londoni kwenda Ikungi kwa muda mrefu hii barabara ilikuwa haipitiki kipindi cha masika, lakini hawa ndugu zetu wa TANROADS wa Mkoa wa Singida kwa kweli walikuwa very proactive, tulikuwa tukiwapigia simu wanakuja kutoa ushirikiano mkubwa sana kwa ajili ya kutengeneza

Mheshimiwa Naibu Spika, pia hii barabara ya kutoka Manyoni kwenda Heka kwenda Sanza kipindi cha masika ilikuwa haipitiki. Hawa ndugu zetu wa TANROAD wa Singinda walitusaidia sana, tulikuwa tunawakuta wamefika site wanakuja kurekebisha. Kilio chetu kikubwa ni hii barabara ya kutoka Manyoni kwenda Heka kwenda Sanza inakuja kutoka Mbambala inakuja kuingia Dodoma, Rais Hayati Magufuli alituahidi kuweka kiwango cha lami, nitapenda kusikia kutoka kwa Waziri anawaambia nini wananchi wa Manyoni sasa hii ahadi ambayo Rais wetu mpendwa hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliahidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, naomba niishauri Wizara, kuna ahadi nyingi sana ambazo zimetolewa na viongozi wetu wakubwa, wengi wamesema kuna ahadi kuanzia Awamu ya Tatu, ya Nne na Tano. Ningeishauri Wizara wafanye mapping ya ahadi zote, unajua hawa wenzetu wakubwa wakishaahidi wananchi wetu wanakuwa na imani kubwa sana. Hivyo, ni vizuri tukatengeneza mapping na tukatengeneza planning ya jinsi gani kila mwaka wataenda kupunguza zile ahadi. Hawa ni viongozi wakubwa, wametumikia hili Taifa, tunahitaji kuwapa heshima, lakini tukumbuke ahadi ni deni. Mbaya zaidi…(Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa, kengele imeshagonga.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru sana na naomba niunge mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nikushukuru sana kwa kunipa hii nafasi. Lakini nitumie nafasi hii vilevile kumpongeza sana Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa sana ambayo anaifanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua kwamba Corona ilikuwa ni janga kubwa lakini mama yetu amekuwa jasiri sasa hivi tuna chanjo Tanzania. Wote tunatambua kwamba Corona imeleta madhara mengi lakini mama yetu ame-fight akapata fedha za UVIKO kutoka IMF na sasa hivi tuna fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua kwamba Tanzania ilianza kusahaulika. Mama yetu sasa hivi anaifungua, sasa hivi Tanzania inajulikana nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitumie nafasi hii vilevile kumpongeza sana ndugu yangu, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Nchemba, pamoja na Naibu Waziri wake kwa kazi ambayo wanaifanya. Nikushukuru sana Waziri kwa kazi mnayoifanya na kuleta rasimu ya huu mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ina mambo matatu ambayo ninapenda kuishauri Serikali. Jambo la kwanza, ninapenda kuishauri Serikali kwenye mfumo wa kukamilisha miradi mikubwa ya maji; la pili, ninapenda kuishauri Serikali kuhusu huduma za afya, hususan paradox iliyopo kati ya zahanati na vituo vya afya; jambo la tatu, ninapenda kuishauri Serikali kuhusu mfumo mzuri wa kutoa mikopo ya elimu ya juu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais wetu, mama Samia Suluhu Hassan. Kwa upande wangu mimi Jimbo la Manyoni Mashariki nina mradi mkubwa sana wa maji wa Kintinku – Lusilile wa takribani bilioni 11, mpaka sasa tumepewa takribani bilioni tano. Na mwaka huu wamenitengea bilioni 2.4 na juzi hela za UVIKO ametupatia takribani milioni 500 kwa ajili ya kukamilisha huu mradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye suala la miradi ya maji nina hoja takribani tatu. Hoja ya kwanza ni kwamba tuna miradi mikubwa ya maji lakini tunatumia muda mrefu sana kuikamilisha. Nitatolea mfano mdogo wa mradi wangu wa Kintinku; mpaka sasa hivi tumesha-spend fifty percent ya bajeti ya eleven billion. Ile fifty percent imeshakaa zaidi ya miaka mitatu. Hiyo ni sunk cost, maana yake kuna wear and tear ambayo inaendelea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kushauri kwenye hili. Cha kwanza, natamani kuona ni jinsi gani Wizara inaweza ikaja na modality mpya ya kuhakikisha kwamba tunakamilisha hii miradi ya maji kwa wakati. Ninapenda kumshauri Waziri mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Nchi za Malaysia, Uturuki, hata Indonesia wanachofanya wameingia kwenye Public Private Partnership na manufacturers wa mabomba. Wanachofanya kwa sababu sisi tunajua kwamba tuna changamoto ya ku-raise hela kwa kutumia taxation, tunahitaji ku-tax ili tu-spend, kinachofanyika hapa, Serikali inaingia kwenye long-term agreement na manufacturers wa mabomba, then tunakuwa tunawalipa by installments.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kufanya hivyo tutakuwa na uhakika kwamba tunaweza tukakamilisha utekelezaji wa hii miradi ya maji ambayo kwa kweli inaweza ikawa na impact kubwa sana. Na kwa kupitia hilo vilevile tunaweza tukaweka incentive. Tunaweka incentive vipi; incentive ya kwanza tunaweza tukawa-exempt hawa manufactures kwa sababu wana-import raw material kutoka nje, wawe na zero tax kwenye importation ya raw material. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii vilevile ita-facilitate viwanda vyetu vya ndani vitakuwa, tutakuza ajira, lakini vilevile tutapunguza ile profit margin ambayo wanaweza wakai-set kwa sababu ya ile payment schedule ambayo tunaweza tukawa tunawalipa hawa manufacturers. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye hili ni kwamba kama tutaenda na huu mfumo wa kutumia private sector waweze kuingia hiyo long-term agreement na Serikali, bado tunaweza tuka-opt kutumia ile force account kwa sababu tayari tutakuwa tuna uhakika wa kupata mabomba, tuna uhakika wa kupata fittings na tunaweza tukatumia force account ili kuhakikisha kwamba tunapunguza tatizo la kutokamilisha miradi kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri huu utaisaidia Serikali kukamilisha miradi mikubwa ya maji ukiwepo Mradi wa Kintinku – Lusilile ambao sasa hivi ni mradi wa zaidi ya miaka 15, bado tunasuasua kuukamilisha. Nina imani kabisa kwamba approach hii itakwenda kuisaidia Serikali.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapenda kushauri upande wa afya. Mimi nitumie nafasi hii kumshukuru sana Rais. Sisi kwa upande wa Jimbo la Manyoni Mashariki kwanza ametupatia milioni 250 za fedha za tozo ambazo tunakwenda kukamilisha Kituo cha Afya cha Chibumagwa, lakini vilevile tunaanza ujenzi wa Kituo kipya cha Afya cha Sanza. Mbali ya hiyo, kwenye hela za UVIKO ametupatia takribani milioni 300, tunakwenda kujenga jengo la dharura. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini mimi nina ishu kubwa mbili upande wa afya. Ishu ya kwanza Sera yetu ya Afya ilikuwa inasema kwamba kila kata tunahitaji kujenga kituo cha afya, lakini kila kijiji tunahitaji kuwa na zahanati. Kulingana na uwezo wa Serikali nadhani suala la kujenga kituo cha afya kila kata sasa hivi siyo wazo ambalo ni realistic. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri nini; la kwanza, mimi naomba nishauri kwamba hatuhitaji kujenga kituo cha afya kila kata, zaidi tunahitaji kujenga vituo vya afya vya kimkakati. Na hivi vituo vya afya viwe clustered ili Serikali iwe kwanza na uwezo wa kupeleka watumishi pale, lakini iwe na uwezo wa kupeleka vifaa, lakini vilevile tutakuwa na uwezo hata wa kusaidia…

MWENYEKITI: Kengele ya kwanza hiyo.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la zahanati; zaidi ya asilimia 70 ya Watanzania wanaishi vijijini. Demand kubwa upande wa afya ipo kwenye zahanati kuliko iliyopo kwenye vituo vya afya. Vituo vya afya ni referral point, mtu akishindwa kwenye zahanati anakuwa referred kwenda kwenye kituo cha afya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo najua utaratibu wa Serikali ni kwamba kila mwaka tunatenga takribani zahanati tatu kwa kila jimbo. Kwa upande wangu na maono yangu naona kwamba zahanati tatu kwa kila jimbo ni chache sana, na kwa sababu tunataka kuhakikisha tunafikisha huduma za afya karibu na wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni nini? Kwanza tunahitaji ku-invest zaidi kwenye zahanati tuongeze zahanati sasa kutoka tatu kwenda angalau sita kila jimbo kila mwaka, lakini kama nilivyoshauri kwamba tutakuwa na zile clustered health facilities ambazo sasa angalau kata tatu zitajengewa kituo cha afya kimoja ili ziwe referral points kwa ajili ya wale wanaotoka kwenye zahanati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ni suala la mikopo ya elimu ya juu. Katika wiki mbili hizi Wabunge wengi tumepokea simu nyingi sana za vijana wetu ambao wamekwenda vyuo vikuu, na katika hili niseme bado ule mfumo wetu wa means testing wa kuwachuja vijana ambao wana uhitaji mimi nauona bado una mapungufu makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hili niseme kwa sabbau gani; bado tunapata simu nyingi za vijana wetu ambao wanatoka kwenye maeneo yetu ambao tunajua kabisa ni watoto wa maskini lakini bado hawajapata mikopo. Na tatizo lililopo vilevile ule mfumo ni very bureaucratic, mtoto wa kijijini ambako mtandao haujafika anatakiwa a-upload, a-apply na aweke documents zote kwenye mfumo. Mimi nashauri mfumo huu ufanyiwe marekebisho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na ni marekebisho gani nashauri; kwanza nashauri tuachane na huu mfumo wa means testing. Na ningeshauri mambo matatu; la kwanza, tuje na mfumo wa category, tuwe na categories tano, category ya kwanza kwa wale wanafunzi waliosoma shule za Serikali form four na form six hawa ningeshauri wapewe mkopo asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, category ya pili ni wale wanafunzi waliosoma kidato cha nne…

MWENYEKITI: Kengele ya pili hiyo.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, mimi nikushukuru sana na ninaunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii, lakini naomba nimshukuru Waziri, Profesa Mkenda pamoja na Naibu Waziri, Mheshimiwa Bashe na Watendaji wote wa Wizara.

Mheshimiwa Spika, nina hoja mbili kubwa, hoja ya kwanza ni kuhusu Mfuko wa Umwagiliaji na hoja ya pili ni kuhusu kilimo cha korosho Manyoni. Kwanza, niishukuru sana Serikali tulianzisha Tume ya Umwagiliaji, kuna Kanuni za Umwagiliaji za 2015, lakini kuna Sheria ya Umwagiliaji na vilevile kuna Mwongozo wa Tozo na Ada za Umwagiliaji, hii ni hatua kubwa sana kwenye sekta ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini niseme kwamba hatuwezi kuendeleza kilimo cha Tanzania iwapo Profesa hutaweka mkazo na uwekezaji kwenye umwagiliaji. Hiyo itabaki kuwa ndoto, naomba tuige nchi za wenzetu Egypt, Somalia, Sudan na nchi zingine ambazo zimeendelea.

Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni nini? Katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki nina skimu zaidi ya 8, nina skimu za Udimaa, Ngait, Mawen, Chikuyu, Saranda, Msemembo, Kintinku na Mtiwe. Hata hivyo, nikipitia bajeti hii, sijaona sehemu ambako Profesa unaenda kuwekeza kuhakikisha kwamba ule uharibifu ambao ulisababishwa na mvua kubwa tunaenda kuwakomboa wakulima.

Mheshimiwa Spika, nina masikitiko makubwa kwa sababu kama hatutawekeza kwenye umwagiliaji…

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Chaya sekunde moja tu, Waheshimiwa Wabunge sasa tumpe nafasi Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mbunge yeyote asiende pale ili apate kusikiliza masuala ya kilimo kwa sababu ni muhimu sana. Anayemhitaji Waziri Mkuu tuna ofisi hapa Administration kuanzia saa 7.00 mchana mpaka saa 11.00 jioni mnaweza mkaenda kumuona. Sasa hivi muacheni ili asikilize hoja za Waheshimiwa Wabunge kuhusu matatizo halisi ya wananchi maana yeye ndiye Kiongozi wa Shughuli za Serikali Bungeni. Mheshimiwa Dkt. Chaya, endelea. (Makofi)

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, hoja yangu ni nini? Mwaka jana katika hizi skimu nyingi za umwagiliaji ambazo ziko katika Jimbo la Manyoni Mashariki zilipata adha kubwa sana ya mvua. Niliwasiliana sana na wenzetu wa Tume ya Umwagiliaji nawashukuru, waliahidi kuja kuturekebishia.

Mheshimiwa Spika, kuhusu Mfuko wa Umwagiliaji, nina hoja kadhaa ambazo napenda kulishauri Bunge. Kwanza huu mfuko ambao tumeuanzisha na umeanza kufanya kazi mwaka jana unategemea ada na tozo za wanachama. Sasa tunategemea huu mfuko uje ujenge skimu kubwa hapa Tanzania lakini unategemea skimu ambazo hazijaendelezwa. Profesa naomba uliangalie hili, tunahitaji kwanza kuwekeza kwenye skimu hizi, kuzirekebisha ili huo mfuko wako utune. Bila kuwekeza kwenye hizi skimu Profesa hizi skimu zitabakia kuwa ndoto na mfuko utabakia kuwa ndoto na umwagiliaji Tanzania utabakia kuwa ndoto. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala lingine hivi vyama vya wamwagiliaji vimeanzishwa lakini havijapewa mafunzo na utendaji wake wa kazi upo chini sana. Napenda kujua Profesa umejipangaje kwenye bajeti yako kuhakikisha kwamba, kwa mfano kwenye zile skimu zangu 8, umeweka bajeti ya kuja kuviwezesha vile vyama vya umwagiliaji, uwape mafunzo, wajue jinsi ya kusimamia mifuko hiyo, jinsi ya kuchanga na hata jinsi ya kuchukua hizo tozo na kurudisha kwenye mfuko wa Serikali. Kwa hiyo, naona hii ni hoja ya muhimu na ningemshauri Waziri aweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni suala la kilimo cha korosho. Mimi naishukuru sana Serikali tumeanzisha kilimo cha korosho na baadhi ya Wabunge wetu humu wengi mna mashamba ya korosho kule Manyoni. Tunatumia block farming system ambapo wakulima wengi wameungana na nimshukuru sana Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni kuhakikisha kwamba kilimo cha korosho kinaenda kuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi tumeanza uvunaji wa awamu ya kwanza wa korosho kule Manyoni. Hoja yangu hapa, nitatamani kusikia kutoka kwa Profesa kwenye bajeti hii, amejipangaje sasa kuhakikisha kwamba Manyoni kilimo cha korosho kinakuwa chenye tija? Je, mnawasaidia vipi watu wa Manyoni kwa kuja na mfumo rafiki sasa kwenye masuala ya masoko, maghala na kuwa na mfumo rafiki kuhakikisha kwamba wale wakulima wawe sasa na matumaini ya zao la korosho?

Mheshimiwa Spika, kuna sintofahamu kubwa sana kuhusu suala la korosho. Nimesikia ndugu zangu wa Mtwara na Lindi wakilalamika, hatutaki hayo makosa yatokee Manyoni na ningetamani kuona sasa Waziri anakuja kwenye bajeti yake na bajeti ambayo Manyoni itakuwa ni sehemu ya kipaumbele kwenye suala la korosho na hasa kipindi hiki ambapo tumeshaanza kuvuna ili wananchi na wakulima wetu wapate matumaini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la miundombinu. Tutatamani kuona Waziri unakuja na bajeti ambayo kwa Manyoni ambapo Bodi ya Korosho inafanya kazi ni jinsi gani mnaenda kuwasaidia…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Chaya, dakika tano ni ndogo.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nami naomba nichukue nafasi hii kukushukuru sana kwa hii nafasi. Kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya. Sisi watu wa Manyoni tunamshukuru sana kwa fedha ambazo ameleta nyingi sana za miradi.

Mheshimiwa Spika, mimi leo nitachangia maeneo makubwa mawili. Eneo la kwanza nitachangia kuhusu Mfuko wetu wa Bima ya Afya ya Taifa, na nitajikita zaidi kwenye suala la matumizi ya TEHAMA. Eneo la pili nitachangia kuhusu mfumo wa ujenzi wa viwanja vya ndege ambao kwa sasahivi kuna mkanganyiko kati ya TANROADS na Wakala wa Usimamizi wa Viwanja vya Ndege Tanzania (TAA).

Mheshimiwa Spika, naomba nianze na suala la bima ya afya. Sasahivi tunaenda kwenye mchakato ambapo tunataka kuja na bima ya afya kwa wote. Naomba nikiri kwamba nimepitia taarifa ya CAG na tumefanya uchambuzi kwenye kamati yetu ta PIC. Sidhani kama Shirika la Bima ya Afya ya Taifa ambalo hili shirika tunalo sasahivi lina uwezo wa kuistahimili kubeba watu takribani milioni 61.

Mheshimiwa Spika, sasa hivi Shirika la Bima ya Afya linahudumia wanufaika takribani milioni 4.6. Kati ya hawa milioni 4.6 milioni 1.2 ni wale wanaochangia. Tunategemea kama tutakuja na Sheria ya Bima ya Afya kwa Wote, hili shirika litahudumia watu zaidi ya 60,000,000.

Mheshimiwa Spika, nikwambie tu kwamba shirika letu linamatatizo makubwa sana na nitaomba niyaseme.

Mheshimiwa Spika, nimepitia taarifa ya CAG, lakini tulipitia taarifa ya TR. Vile vile tulifanya uchambuzi kwenye kamati yetu. Shirika hili lina matatizo makubwa matatu. Kwanza, tulitegemea hili shirika liweze kujikita zaidi kwenye matumizi ya TEHAMA. Shirika linatumia kwa kiwango kidogo sana TEHAMA, hususan maeneo ya vijijini. Lingine, kuna udanganyifu mkubwa sana kwenye utoaji wa ile huduma, hususani kwenye matumizi ya kadi. Nitatolea mfano baadae. Jambo la tatu, tulitegemea shirika lingejikita zaidi katika kukusanya madeni, hata hivyo Shirika halijaweza kukusanya madeni. Kuna madeni mengi sana ya zaidi shilingi bilioni 10 yapo nje, na tunategemea hili shirika lijikite kweye uwekezaji; litaweza kuwekeza vipi kama halina capacity ya kukusanya madeni?

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho, hoja yangu ni kwamba, tunategemea mbali ya kwamba hili shirika lengo lake ni kusajili wanachama na kutoa huduma, lakini linahitaji kujikita katika kuwekeza. Uchambuzi wetu tulioufanya kwenye Kamati ya PIC, tuliona kwamba kama itaenda na trend hii nadhani uwezo wake wa kuwekeza utakuwa mdogo sana.

Mheshimiwa Spika, nilifanya uchambuzi wa taarifa ya CAG. Katika taarifa ya CAG, nitatoa mfano. Kuna wafanyakazi 2,495 wa sekta binafsi ambao wanatoka katika kampuni 87, hawa walisajiliwa kama wafanyakazi wa umma. Hili ni tatizo kubwa sana la mfumo wa TEHAMA. Jambo lingine, taarifa ya CAG inasema kuna wanachama 165 ambao kimsingi sheria inasema wale wategemezi wasizidi watano, lakini wanachama zaidi ya 165 walikuwa na wategemezi ambao wamezidi kiwango kile ambacho sheria imesema. Hili ni tatizo kubwa la mfuko.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kwamba kuna wategemezi 73 waliosajiliwa kama wachangiaji. Hili pia ni tatizo kubwa sana la mfumo wetu wa TEHAMA. Mbali na hiyo, taarifa ya CAG, inasema kwamba kuna wanufaika 731, ambao ni wanaume walipata huduma ya upasuaji wa kujifungua, na haya malipo yalillipwa. Naomba nirudie, taarifa ya CAG, inasema, kuna wanufaika 731, wanaume walipata huduma ya kujifungua na haya madai yakapelekwa NHIF yakalipwa. Hili ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ni kwamba, kuna wanachama 444, walipata huduma ya full blood picture zaidi ya mara moja kwa siku. Narudia tena, kuna wanachama 444, walipata huduma ya picha kamili ya damu, yaani full blood picture zaidi ya mara moja kwa siku ndani ya siku 30. Hili ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, kulingana na kanuni za NHIF, ni kwamba mwanachama akipewa miwani mara moja kwa mwaka, hatakiwi kupewa miwani tena. Madai yaliyopelekwa na wanachama, kuna wanachama walipata miwani zaidi ya mara moja ndani ya mwaka mmoja. Hili ni tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Spika, kuna tatizo lingine kubwa. Nimepitia taarifa ya CAG. Katika taarifa ya CAG, kwanza kuna madai ambayo yalikataliwa kabisa na shirika la bima. Kwa mfano, madai kutoka Muhimbili na madai kutoka Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete zaidi ya Shilingi bilioni 3.87 yalikataliwa. Sababu ya kukataliwa ni kwamba kuna kughushi na taarifa zisizo rasmi. Ndiyo maana nimesema kama tunataka hili shirika ndiyo libebe bima ya afya kwa wote, kama tu hii asilimia nane, kwa sababu sasahivi linachukua asilimia nane ya watu wote, je, tukimpa asilimia 100, zaidi ya watu milioni sitini, hili shirika linaweza likastahimili? Kwa hiyo tuna matatizo makubwa sana

Mheshimiwa Spika, zaidi ya hiyo ni kwamba, katika mwaka wa 2019 na 2020, shirika lenyewe llilikataa zaidi ya madai ambayo yanatakribani shilingi bilioni tatu, madai ambayo wenyewe waliyakataa, kwamba haya ni madai ambayo ni batili. Kwa hiyo hii inaonesha kabisa kwamba tuna matatizo makubwa sana kwenye shirika letu.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine, shirika limeshindwa kukusanya zaidi ya shilingi bilioni 11. Tunategemea shirika liende likawekeze lakini linadai taasisi za umma zaidi ya shilingi bilioni nane na linadai taasisi za sekta binafsi zaidi ya shilingi bilioni mbili, zipo nje hawajalipa na tunategemea hili shirika lijiendeshe. Haya ni matatizo makubwa sana.

Mheshimiwa Spika, ninashauri; kwanza hili shirika tunategemea tulipe mzigo mkubwa baadaye wa kusimamia bima ya afya kwa wote, lakini tumeona halina uwezo wa kukusanya madeni na wakati huo huo mfumo wa TEHAMA bado unasumbua sana. Nashauri kwamba tulifanyie restructuring hili shirika Ili tunapokuja na hoja kwamba linahitaji kubeba bima ya afaya kwa wote liwe na uwezo wa kubeba bima ya afaya kwa wote.

Mheshimiwa Spika, la pili ni kwamba tumeona kuna matatizo makubwa sana ya TEHAMA hususan maeneo ya vijijini ambako hakuna mitandao, na kuna muda ambapo kama hakuna mtandao ndani ya masaa 24, wanatakiwa wawe wamesha-submit zile claims zao na wakishindwa ku-submit, system ina-reject. Kwa maana hiyo mimi nashauri; kwamba tunahitaji vile vile kuangalia ule mfumo wa TEHAMA, upitiwe upya na hivyo uweze kuwa na tija.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo nitachangia leo ni kuhusu mfumo wa ujenzi wa Viwanja vya Ndege.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2016 Serikali iliamua kuhamisha majukumu ya ujenzi wa viwanja vya ndege kutoka TAA (Wakala wa Kusimamia Viwanja vya Ndege) kwenda TANROADS.

Mheshimiwa Spika, Serikali ilikuwa na nia njema, lakini nadhani umefika muda muafaka sasa, tumejitathmini. Sisi tumechambua ndani ya Kamati yetu, tukaona kwamba bado ni muda muafaka ambapo majukumu ya kujenga viwanja vya ndege yarudi TAA.

Mheshimiwa Spika, kwanini tunasema hivyo? Ukiangalia international standards zina-guide kwamba, wataalamu wengi wa kujenga viwanja vya ndege, wa kutoa guidance wapo TAA. Tunatambua kwamba kweli tuna wataalamu wetu wapo TANROADS, lakini wale wengi wamebobea kwenye ujenzi wa madaraja, barabara na mambo mengine. Kwa hiyo hii imekuwa hoja; na kuna muda ambapo wakati vile viwanja vinatengenezwa vinakuwa havina zile international standards.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo mimi…

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Dkt. Chaya kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Ulenge.

T A A R I F A

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante. Naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba; si tu hilo la kupora miradi kutoka TAA kuipeleka TANROADS, lakini pia chanzo kikuu cha mapato kwa TAA ni passenger service charge, ambayo dola 40 kwa kila anayepanda ndege za kimataifa, na shilingi 10,000 kwa kila anayepanda ndege za ndani. Fedha hizi zote zinakimbizwa TRA wakati TCAA, kampuni ambayo inafanya kazi zinazolandana na TAA, wanakusanya na kufanya miradi yao ipasavyo. Kuna nini kutokuiamini TAA kufanya kazi zake ipasavyo? Hiyo ndiyo taarifa niliyotaka kumpa.

SPIKA: Hilo swali anapswa kulijibu Serikali au anapaswa kulijibu mwenyekiti wa Kamati. Maana unayempa taarifa ni yeye, atamuuliza nani swali sasa maana yeye ni mjumbe wa Kamati?

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, nimeongezea tu mchango wake in terms ya taarifa kwamba siyo hilo, kuna hili lingine pia linaibana TAA.

SPIKA: kwa maana nyingine ni kwa ajili yako na wengine. Yaani hizi hoja ni hoja zetu sisi kama Bunge. Kwa hiyo ukiuliza swali ni kwamba mwenyekiti. Kama swali alilokuwa anauliza Mheshimiwa Mpina maana yake mwenyekiti wa kamati atakapokuja kuhitimisha ataanza kujibu yale maswali. Kwa hiyo wewe umeeleweka na Mheshimiwa nadhani pia ameshakuelewa hoja yako.

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa mwongozo wako.

SPIKA: Karibu sana.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa huo muongozo…

SPIKA: Mheshimiwa Chaya, subiri kidogo. Mheshimiwa Chaya unaipokea taarifa hiyo?

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, naipokea na ninashukuru kwa ufafanuzi wako.

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotangulia kusema kwamba nia ya Serikali ya kuhamisha ujenzi wa viwanja vya ndege kutoka TAA kupeleka TANROADS kipindi kile haikuwa nia mbaya. Hata hivyo ndhani muda muafaka umefika sasa kwamba turudishe yale majukumu kutoka TANROADS tuyarudishe TAA, na nimetoa sababu za msingi. Kwanza watu wa TAA ndiyo wana-guide zile international standards za ujenzi wa viwanja vya ndege, wana wataalamu ambao wapo TAA, wanye ubobezi kwenye masuala ya ndege na kadhalika.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba TANROADS tuna wabobezi wengi sana kwenye kujenga barabara na madaraja. Kwa hiyo tumeliona hili na tumelijadili katika Kamati yetu. Tunaishauri Serikali, muda muafaka umefika sasa kurudisha yale majukumu ambayo tuliyapeleka TANROADS yarudi TAA ili basi TAA iwe na majukumu kamili ya kuhakikisha, kwamba wanajenga vile viwanja vya ndege, wanasimamia viwanja vya ndege na vile vile wana-provide ile maintenance kwa ajili ya viwanja vya ndege.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, narudia tena kushukuru sana kwa nafasi uliyonipa na ninaunga mkono hoja. (Makofi!)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia kwenye hii Wizara muhimu, Wizara ya Elimu. Kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambazo anazifanya hususani katika Jimbo la Manyoni Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Profesa Mkenda pamoja na Mheshimiwa Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanazozifanya. Mwaka huu manyoni tumepewa chuo cha VETA, na nilikuwa nikiuliza sana swali la VETA, mwaka huu tuna ujenzi wa Chuo cha VETA Manyoni, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nimshukuru vilevile Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu, Profesa Carolyne, mwalimu wangu wa Chuo Kikuu cha Sokoine. Nimshukuru sana pia Kamishna wa Elimu, Mkurugenzi wa TEA na Mkurugrnzi wa Bodi ya Mikopo. Mkurugenzi wa Bodi ya Mikopo tulikuwa tunapata vilio vingi sana vya vijana wetu lakini kwa kweli mwaka huu mmetutendea haki sana. Kwa hiyo nakushukuru Mheshimiwa Waziri lakini nampongeza sana Mkurugenzi wa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Dkt. Badru vile vile kwa kazi kubwa ambayo ameifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nina hoja mbili. Hoja ya kwanza nitazungumzia kuhusu hii Taasisi ya Elimu ya TEA (Tanzania Education Authority), lakini ya pili muda wangu ukiniruhusu nitachangia kuhusu mfumo wa elimu yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Taasisi yetu ya Elimu TEA, kwanza nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri kwa kupitia TEA. Tumeona kupitia TEA tumekuwa na programu mbili. Programu ya kwanza ni kupitia ule Mfuko wa Elimu, mmekuwa mki–compliment juhudi zinazofanywa na TAMISEMI kwa kujenga vyumba vya madarasa na kujenga vyoo kwenye shule zetu, na huu ni ubunifu mkubwa sana. Tusitegemee tu TAMISEMI waweze kuweka miundombinu kwenye taasisi zetu za elimu. Lakini Profesa umeliona hili, kuna maeneo ambayo yalikuwa yamesahaulika. Mkigundua lile eneo limesahaulika nyinyi mna-top up kwa kutumia taasisi ya elimu TEA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili, hawa wenzetu TEA vile vile wamepewa dhamana ya kuendesha yale mafunzo ya elimu ya ufundi wakishirikiana na VETA na vyuo vyetu vya ufundi. Taarifa niliyonayo ni kwamba zaidi ya vijana 45,000 wameshapata mafunzo haya, na sisi kwa Manyoni tumepata vijana wengi sana. Mpaka kwa sasa hivi nadhani wanafika Zaidi ya vijana hata 400 ambao wamepata haya mafunzo kwa kupitia huu mfumo wa TEA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ushauri wangu ni nini kwenye taasisi hii ya TEA; tumeona impact kwa kupitia hiyo miradi ambayo mnajenga vyoo na madarasa kwenye maeneo ambayo TAMISEMI hawajagusa, lakini tumeona impact kwa kupitia fedha mnazotoa kwa ajili ya kuwapeleka wale vijana wetu wanapata elimu ya ufundi. Ni muda muafaka sasa kuijengea uwezo TEA, kuiongezea nguvu na bajeti ili waweze kuongeza vijana wengi. Pia tunatamani yale maeneo ambayo TAMISEMI haijaweza kupeleka miundombinu kwa kupitia Wizara yako Mheshimiwa Mwenyekiti lakini vilevile profesa ongezeni bajeti ili TEA waweze kufanya mambo makubwa zaidi. Kwa jhiyo kwa upande wa TEA mimi ningeshauri hayo mawili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni kuhusu mfumo wetu wa elimu na concept ya kujiajiri. Tupo kwenye mapitio ya mfumo wetu wa elimu, kutengeneza mitaala na vile vile kuhuisha sera yetu ya 2014 ambayo kimsingi haijawahi kufanya kazi. Lakini ningetaka kujiuliza na tujiulize wote sisi kama nchi tunataka nini kwa kupitia elimu yetu ya Tanzania? Nadhani hili ni suala la msingi sana ambalo ni lazima tujiulize.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mawazo ya aina mbili yanayokinzana. Wengi tunafikiri kwamba tunahitaji kuwatoa vijana vyuoni waende wakajiajiri. Lakini tukumbuke vile vile kwamba tunahitaji vijana hawa waingie kwenye soko la ajira, hususani soko rasmi Serikalini lakini hata kwenye private sector. Lakini hoja hii ya kujiajiri vilevile inatafsiriwa toifauti, na hili niliseme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kijana amesoma IT, lakini wengi ukisikia wanaongelea concept ya kujiajiri anakwambia huyu kijana aende akafuge, Profesa ume-invest miaka minne kwa kijana amesoma IT unaenda kumwambia ajiajiri, nadhani that is a very serious mismatch. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea Profesa utuambie kwamba huyu kijana akajiajiri kwenye area his of specialization. Kama amesoma IT tuje na micro business ambazo atatumia ujuzi wake wa IT; na mimi hapo ndipo nilipotaka niweke hoja yangu. Kwa nini nasema hivyo; ni kwamba hawa vijana wengi tunapowahamisha kwenye areas of their specializations, matokeo yake wanakuwa hawana matamanio ya kukaa kwenye zile field. Atakaa kwa muda tu baadaye atakata tamaa. Atatamani siku zote arudi kwenye eneo ambalo alilisomea, kwa hiyo ni eneo ambalo mimi nadhani tunahitaji vilevile kuliangalia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo lingine ambalo nilitaka kuliangalia vilevile ni suala la mapitio ya huu mtaala. Kwenye mapito ya mtaala mmesema kwamba mnataka kuanza kuondoa mtihani wa darasa la saba. Sasa Profesa Mkenda tunaenda kuondoa mtihani wa darasa la saba, tutawapimaje walimu wa shule za msingi? Tunawezaje kuhakikisha kuna accountability kwa walimu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ningeshauri; ule mtihani wa darasa la saba bado ni muhimu unatakiwa uendelee ili tuweze kuwapima uwajibikaji walimu . Tunapoutoa maana yake mwalimu ataona hamna maana yoyote yeye kufundisha wala kuingia darasani kwa sababu hakuna kipimo chochote. Kwa hiyo bado ningeshauri kwamba ule mtihani uendelee ili tuweze kujua ni vijana gani na vijana wa aina gani ambao tunawapeleka huko juu kwa ajili ya kusoma kwa upande wa sekondari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine, tumekuja na hoja nzuri sana, tunataka ku-integrate masomo ya amali na ufundi sekondari; na niliongea siku moja tulikuwa na kikao chetu pale, mimi nikasema kwamba sawa, ni wazo jema tunataka kupeleka sekondari vijana wetu wapate elimu ya ufundi; lakini Profesa bahati nzuri wewe umefundisha Chuo Kikuu cha Dar es salaam mimi nimefundisha Chuo Kikuu cha Dodoma. Lengo la elimu ya msingi ni kutoa general knowledge. Inamuandaa mtu ili baadaye akienda vyuoni aende akasome masomo ambayo yatampa ujuzi, yatampa skills. Kwa hiyo katika level ya shule za msingi na sekondari hatutengenezi skills, pale tunamuandaa mtu ili baadae anapoenda chuoni aweze kuwa na knowledge ya kutosha ili tumjengee skills.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ok, tumekeja na concept kwamba tunataka sasa katika level ya sekondari hawa vijana wafundishwe ujuzi ili weweze kutengeneza let say washone nguo, waweze labda kutengeneza keki na vingine, ni jambo jema, lakini bado mimi nikasema kwamba sasa hivi Serikali inawekeza kwenye VETA, kwa nini sasa tusifikirie badala ya kusema kwamba tutapeleka mzigo mkubwa sekondari ambao vijana wengi tunawaandaa kwa zile general knowledge, kwa nini tusiweke nguvu kwenye VETA ambazo mmezianzisha ili wale wanaoshindwa darasa la saba, wameshindwa kuendelea sekondari hawa iwe lazima kwenda kwenye hivi vyuo vya ufundi? Na kwamba wale watakaoshindwa kutoka form four Kwenda form five hawa ndio iwe lazima Kwenda kwenye vyuo vya ufundi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine tukumbuke, sio kila mtu lazima awe fundi bado tunahitaji wahasibu, tunahitaji watu wa manunuzi. Kuna watu watastaafu, kuna watu Mungu atawachukua, kuna watu wataacha kazi kwa hiyo haitafika siku kwamba hii nchi yote inahitaji mafundi tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, bado tunahitaji walimu , mainjinia, madaktari na watu wengine. Kwa hiyo mimi niliona, ni kwamba tunapofanya mapitio ya ule mtaala tuangalie kwamba sawa tunaweka masomo ambayo yatakuwa na ubunifu lakini tusisahau kwamba katika level ya sekondari si level inayomuandaaa mtu kuwa poroductive, hapana. Level ambayo inamuandaa mtu kuwa productive ni level ya Chuo Kikuu tu, na ndiyo maana tunataka wakitoka pale wa- accelerate Kwenda vyuoni tuimarishe vyuo vya VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni nini; kwanza mimi nashauri mtihani wa darsa la saba uendelee, uendelee kwa sababu tunahitaji kuwapima walimu uwajibikaji wao. Tukiondoa mtihani wa darasa la saba haitakuwa na maana ya kuwa na walimu shule za msingi, hawatawajibika. Hilo ni eneo la kwanza. Lakini la pili, kwa wale ambao hawatabahatika Kwenda kidato cha kwanza na kwa wale ambao hawatabahatika Kwenda kidato cha sita kutokea kidato cha nne, sasa hapa ile elimu ya ufundi ndipo iwe ya lazima. Kwa sababu hawa hawawezi Kwenda hata vyuo vingine vya kati hawa sasa tuwarudishe kwenye vyuo vya ufundi ambavyo tumevijenga, na iwe ya lazima huo ni ushauri wangu wa pili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine, niliwahi kuongea huko nyuma, na Waheshimiwa Wabunge wengi wamelaalmika hapa, kwamba kuna tatizo sana kwenye competences za walimu wetu. Lakini tatizo, Profesa, na umefundisha Chuo Kikuu cha Dar es salaam, ukifuatilia wanaoenda kusomea ualimu ni mtu aliyepata four, three ndio wanaoenda kusomea ualimu. Wale waliopata division one na two wanaenda kusoma kozi zingine, iweje wewe ulipata three umtengeneze mwenzako apate division one? Kwa nini tusibadilishe mfumo, kwamba wale waliofaulu zaidi kwa division one na two ndio watufundishie watoto wetu? Lakini wale tumewaacha wamekimbia wameenda kusoma wanakuja kufanya masomo ya business. Kwa hiyo ni eneo mimi nadhani mnahitaji kuliangalia kwenye sera yetu, kwamba vijana waliofaulu zaidi tuweke motisha ili waone ualimu ni mzuri, waweze kurudi kufundisha kule watutengenezee brains zingine huko katika nanii zetu. Lakini lingine…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MWENYEKITI: Ahsante sana Mheshimiwa Chaya.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nakushukuru, naunga mkono hoja.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nakushukuru kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia leo kwenye bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani lakini kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kaka yangu Engineer Masauni lakini Naibu Waziri kaka yangu Sagini kwa kazi kubwa mnayoifanya. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Rais kule kwetu Manyoni amefanya mambo makubwa sana. Ameleteta miradi mingi sana lakini vilevile ametusaidia sana kwenye upande wa Jeshi la Polisi. Ninamshukuru vilevile Katibu wa Wizara ya Mambo ya Ndani na Naibu Katibu Mkuu kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya kwa Taifa letu lakini ususani katika Jimbo la Manyoni Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo na maeneo mawili takayoenda kuchangia. Eneo la kwanza tachangia upande wa Jeshi la Polisi lakini nafasi ikininiruhusu tachangia kuhusu Jeshi la Zimamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nimshukuru vilevile RPC wa Mkoa wa Singida Afande Stella. Kwa kweli huyu dada yetu ametusaidia sana sisi Manyoni. Manyoni kulikuwa na mauaji yaliyokuwa yakiendelea, niliongea hapa Bungeni, lakini vilevile Mheshimiwa Waziri ulitoa maagizo kwa Afande Stella na ukafanya mabadiliko pale Manyoni. Tumepata OCD mpya lakini na taarifa tayari mmeleta mmpelelezi bado hajafika. Kwa hiyo nimshukuru sana Afande Stella lakini kipekee nikushukuru sana Waziri na Naibu Waziri kwa kulichukua hili kwa umakini kabisa na hali ya usalama Manyoni inaendelea kuimairika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini upande wa Jeshi la Polisi kuna suala la Vituo vya Polisi vya Kata. Wenzangu wametangulia kusema, Mheshimiwa Idd ameongea hapa, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki maeneo mengi kwanza hayana Vituo vya Kata vya Polisi lakini Vituo vya Kata vingi vya Polisi ni vibovu na ni vichakavu. Kwa mfano na Kituo cha Kata cha Sanza ni kibovu sana, lakini hata pale Heka ni kibovu sana. Mbaya zaidi nilishawahi kuchangia hapa Bungeni, katika Kata ya Kintinku pale Askari na Polisi wanatumia gala la EFAD kama kituo cha polisi. Hii ni aibu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikuombe kaka yangu Engineer Masauni, naomba unisaidie tuanze na hili la Kituo cha Polisi katika Kata ya Kintinku. Lakini pia nina Kata zaidi ya nane ambazo hazina vituo vya polisi, zikiwemo Kata za Sasilo, Chikola, Makutupora, Kata ya Saranda na Kata ya Majiri. Nafasi itakapo ruhusu niwaombe basi na hizi kata nazo tuweze kuziangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini lingine kwenye hii Kata ya Kintinku ulimuagiza RPC, Afande Stella; alishafika katika Kata ya Kintinku akakagua eneo wananchi wametenga ekari tatu kwa ajili ya ujenzi wa kituo cha polisi cha kata. Kwa hiyo tayari sisi tuna eneo ekari tatu na Naibu Waziri uliniaidi utakuja kuliona hilo eneo, bado ujatimiza kaka yangu Sagini; nakuomba ufike ili uweze kuliona hilo eneo. Lakini ningeomba kwenye bajeti ya mwaka huu twende tukawajengee kituo cha polisi katika Kata ya Kintinku lakini mnifikirie vilevile kwenye kata hizo zingine nilizozitaja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni uhaba wa vitendea kazi upande wa polisi. Katika Wilaya ya Manyoni kulikuwa na mauaji sana yaliyokuwa yakiendelea lakini hali imeanza kutulia RPC wa Mkoa alimua kuchukua gari kutoka Mkoani kulileta Manyoni kwa sababu Manyoni hawana gari. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, itakapotookea fursa ya magari utuletee gari la polisi Wilaya ya Manyoni ili liweze kusaidia katika doria mbalimbali. Lakini vilevile umesema hapa mnaende kununua pikipiki kwa ajili ya vituo vya kata. Naiomba hiyo fursa vilevile kwenye vituo vyangu vya kata vya polisi ili anagalau tuweze kupata hizo pikipiki ziwasaidie ndugu zetu na watu wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni kuhusu Jeshi la Zimamoto. Kaka yangu Shabiby ameeleza hapa, na mimi naomba niongee hili. Mheshimiwa Rais anazunguka duniani kutafuta wawekezaji. Ile Filamu ya Royal Tour imeleta wawekezaji wengi sana, watu wamekuja wanawekeza. Lakini tuna tatizo moja, zimamoto ya Tanzania ni kama mtoto yatima, amesahaulika ndugu zangu. Unaenda kwa mfano mkoani pale tuna gari moja la zimamoto nalo ni bovu. Sisi tuna wilaya takribani sita, hakuna hata gari moja kwenye wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kwenye Jimbo langu la Manyoni nina miradi mikubwa. Tuna ujenzi wa shule ya wasichana ya bilioni nne, tuna mradi wa bilioni 12 wa maji, lakini tuna ujenzi wa VETA tumepewa 1.4 bilioni; hii miradi inajengwa, it’s very risk, hatuna zimamoto pale Manyoni, wamejenga kaofisi utafikiri banda la kuku. Mheshimiwa Waziri naomba ufanye mageuzi kwenye Jeshi la Zimamoto. Huu uwekezaji ambao mnauleta hatutatengeneza confidence kwa wawekezaji kama mtu anakuja kuweza billions of moneys halafu hakuna uhakika wa Zimamoto, it’s so risks. Kwa hiyo nikuombe kaka yangu Engineer naomba sasa mkatoa kipaumbele sana kwenye Jeshi la Zimamoto huko ndiko ambako tunahitaji kutengeneza confidence kwa wawekezaji. Mwekezaji anapokuja akagundua kwamba tuna Zimamoto, tuna mifumo ya zimamoto, tuna magari tuna ofisi, tunawafanyakazi anakuwa na uhakika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna pigana kujenga viwanda kila eneo lakini unakuta maeneo mengi hayana zimamoto. Kaka yangu pale Shabiby amesema Gairo pale, hapa penyewe mjini ametolea mfano, tuna majengo mengi ya Serikali kule Mtumba, lakini tukiuliza mifumo ya zimamoto, magari ya zimamoto ni machache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimamoto ni mtoto yatima, sasa tunataka asiendelee kuwa mtoto yatima, kwa sababu Rais amepeka nguvu nyingi kwenye uwekezaji, tunahitaji kuweka nguvu nyingi na sisi katika kuimarisha Jeshi la Zimamoto… (Makofi)

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Chaya, taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Saashisha.

TAARIFA

MHE. SAASHISHA E. MAFUWE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nataka nimpe taarifa tu kwamba hapo awali miaka ya 80 Jeshi la Zimamoto lilikuwa linasimamiwa na local government, kwa maana ya uendeshaji wake ulikuwa chini ya TAMISEMI. Tumeisha shauri hapa nyingi; kama huku imeshishindikana basi bora warudishe kwenye halmashauri hizi zenye nguvu ili waweze kuhudumia chombo hiki na ufanisi uweze kuonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitaka kumpa taarifa hiyo tu. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Chaya taarifa unaipokea?

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa hiyo taarifa lakini bado mimi nisinge shauri lirudi halmashauri. Bado Wizara hii hii ya Mambo ya Ndani inayo uwezo wa kusimamia hiki kitengo cha zimamoto kwa sababu uwezo wanao, watalamu wanao, tukipeleka huko halmashauri tunaweza tukaleta matatizo mengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi bado naendelea kuishauri kwamba tunahitaji kuhakikisha tunaweka nguvu sana kwenye Jeshi la Zimamoto. Huu uwekezaji ambao tumesema tunawekeza Mama Samia amezunguka nchi nzima anavutia wawekezaji wamekuja Tanzania, wanaweka viwanda, wanaweka mitambo lakini hatuna mifumo mizuri ya Zimamoto kwa hiyo niombe Serikali sasa katika bajeti hii na bajeti ijayo… (Makofi)

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Chaya kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Esther Matiko.

TAARIFA

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimi Mwenyekiti, nilikuwa nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Dkt. Chaya kwamba ingefaa kwa zile Majiji au halmashauri zenye uwezo waweze kuchukua hili suala la Zimamoto maana yake tumeo fedha tunatenga kwenye Wizara lakini haziendi. Kwa hiyo ukiacha ile pesa ya Mambo ya Ndani tutaendelea kuona rasilimali za Watanzania zikiteketea kwa sababu hatuna vyombo vya zimamoto, kwenye Halmashauri zenye uwezo zipewe jukumu la kuwa na hizi zimamoto, zitasaidia sana. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Mheshimiwa Dkt. Stephene Chaya taarifa unaipokea?

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa hiyo taarifa na nakubaliana na Esther Matiko kwamba kwa Majiji ambayo yenye uwezo wa kununua hii mitambo ya zimamoto wanaweza wakanunua lakini bado hili ni jukumu la Wizara, ninaamini kaka yangu MheshimiwaMasauni bado hajashindwa na ndiyo maana namshauri sasa, kwenye bajeti hii tunataka kuona mnaenda kuwekeza kwenye zimamoto. Wizara mna uwezo wa kusimamia hii sekta, tunataka uwekezaji mkubwa ambao Mheshimiwa Rais anavutia sasa hivi, tutengeneze confidence kwa wewekezaji, hakuwezi kuwa na confidence kwa wawekezaji kama kuna risk kubwa hususana kwenye suala la zimamoto, kwamba mifumo yetu ni mibovu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo mimi niendelee kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri, kwakweli kaka yangu Masauni unafanya kazi nzuri sana. Kwanza ni msikivu, pia Mheshimiwa Naibu Waziri ni msikivu, mara nyingi unapokea simu zetu unajibu meseji hata usiku. Baada ya kusema haya naunga mkono hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Masuala ya UKIMWI kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa nafasi hii uliyonipatia. Vilevile nichukue nafasi hii nimshukuru Rais wetu, Mama Samia, pia nimshukuru Waziri wa Afya na Naibu Waziri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitajikita kwenye magonjwa yasiyoambukizwa. Takwimu zinatuambia kuwa zaidi ya asilimia 40 ya Wabunge humu wamewahi kuvuta sigara, aidha kwa kukusudia au kwa kutokusudia. Vilevile kidunia takwimu inatuambia kwamba zaidi ya asilimia 70 ya vifo vinavyotokea duniani ni kwa sababu ya magonjwa yasiyoambukizwa. Kwa Tanzania, zaidi ya asilimia 40 ya vifo vinavyotokea vinasababishwa na magonjwa yasiyoambukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nasema hivi? Tatizo la magonjwa sasa hivi ni kubwa saba. Wakati UKIMWI unaanza miaka ya 1980 tuliona ni janga kubwa sana la kitaifa, lakini naomba niseme kwamba sasa magonjwa yasiyo ya kuambikiza ikiwemo kansa, ugonjwa wa moyo pamoja na ugonjwa wa figo, ni hatari sana na ni janga la kitaifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikwambie burden ya magonjwa haya ya kuambukiza, nitatolea mfano mmoja tu kwenye ugonjwa wa figo. Wakati tunakwenda kupeleka wagonjwa wetu kutibiwa India kwa ajili ya dialysis na hususan kubadilishiwa figo tulikuwa tunatumia takribani milioni 60 kwa mgonjwa mmoja. Baada ya kuboresha huduma zetu za afya na tunamshukuru Rais, sasa hivi tunatumia takribani milioni 20, ambayo bado ni tatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika wiki moja kuna session nne za kufanya dialysis, kusafisha figo kwa mgonjwa wa figo. Kila session moja inatumia si chini ya 200,000. Kwa hiyo, kwa wiki nzima mgonjwa wa figo anahitaji 800,000 ili afanyiwe usafishaji wa figo. Hili ni zoezi routine mpaka pale Mungu atakapomwita. Tatizo la magonjwa ya kuambikiza is a burden, ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni kwamba bado takwimu, hata hii ninayoisema ya asilimia zaidi ya 40 bado iko under-reported. Kuna watu wengi sana wapo vijijini ambao wameathirika na magonjwa haya yasiyo ya kuambukizwa lakini hatujawatambua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ushauri wangu; natambua kwamba kuna initiatives mbalimbali zimechukuliwa kitaifa na kimataifa. Katika level ya kimataifa tuna Global Action Fund 2020/2025 ambayo lengo lake ni kupunguza magonjwa yasiyoambukiza kwa asilimia 25 ifikapo mwaka 2025. Katika ngazi ya Taifa tuna mkakati wetu wa kitaifa wa kupunguza haya magonjwa yasiyoambikiza. Tumeanzisha mwongozo wa kitaifa wa kufanya mazoezi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina mambo mawili ya kushauri. La kwanza, naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri wa Afya, tuboreshe na tuhuishe DHS2, mfumo wa kukusanya taarifa. Ule mfumo wa kukusanya taarifa una taarifa chache sana zinazoonesha watu wangapi wanaumwa magonjwa yasiyoambukizwa. Hiyo inasababisha tunatoa report ambazo ni under reported, tunaacha watu wengi sana ambao tungeweza kuwasaidia kupata huduma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, hili ni kwa upande wa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Naishauri Serikali; suala la magonjwa yasiyoambikizwa ni multisectoral, ni suala mtambuka. Kuiachia Wizara ya Afya kushughulika na magonjwa yasiyoambukizwa inasababisha tunashindwa ku- deal na tatizo hili. Nishauri sasa, kwamba Mheshimiwa Waziri Mkuu alichukue hili ili liwe kwenye ofisi yake na tuanzishe tume kama tulivyoanzisha Tume ya UKIMWI ili tuweze kuratibu wadau wote ambao wanahusika katika kusaidia suala la kupambana na magonjwa yasiyoambukizwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja, ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwanza mtihani wa darasa la saba usifutwe kwani hali hii itafanya walimu wasiwajibike. Wale ambao hawatafanikiwa kuendelea na kidato cha kwanza waingie kusoma masomo ya ufundi na iwe kwa mseleleko.

Pili, wahitimu wa kidato cha nne na darasa la saba ambao hawatafanikiwa kufaulu vigezo vya kusonga mbele hawa iwe lazima waingine elimu ya ufundi.

Mheshimiwa Spika, tatu, walimu wa kufundisha elimu ya msingi na sekondari ifundishwe na mwalimu ambaye alipata division one au two kidato cha nne na sita. Walioko makazini wataendelea kujiendeleza.

Mheshimiwa Spika, nne, Serikali ianzishe Wizara ambayo itasimamia mambo ya kujiajiri vijana ambayo itaitwa Ministry of Self Employment and Micro Business.

Mheshimiwa Spika, Serikali ipitie umri wa kustaafu uwe miaka 55 ili kutoa fursa ya vijana walioko mtaani kutumikia Taifa wakiwa na nguvu na kupata muda wa kujiajiri.
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii ya kuweza kuchangia kwenye rasimu ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka Mmoja. Nitajikita zaidi kwenye suala la kilimo, lakini muda ukiniruhusu nitajikita kwenye jinsi gani tunaenda kusimamia mapato ya ndani ya halmashauri zetu ili yatumike kwenye ile miradi ya maendeleo, ile asilimia 40.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji wengi wameelekeza hapa, taarifa ambazo Dkt. Mwigulu ame- present hapa, zinaonyesha kwamba kilimo kinachangia takribani asilimia 3.9 kwenye pato la Taifa lakini sekta ndogo ya sanaa imechangia karibia asilimia 19 kwenye pato la Taifa, madini yanachangia asilimia 9.6 na biashara inachangia asilimia 3.5. We are not serious. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo kinachukua zaidi ya asilimia 65 ya Watanzania wameji-engage kwenye kilimo. Sasa hivi watu tulionao ni takribani milioni 61, asilimia 65 ya milioni 61 ni takribani watu milioni 40, wapo kwenye shughuli za kilimo. Sasa kama kilimo kinachangia only 3.9 percent kwenye pato la Taifa maana yake kwa mwaka ni watu milioni mbili tu ndio wanaji-engage kwenye kilimo. Ndio maana nilisema kwamba we are still not serious, tunahitaji kuipa kipaumbele Sekta ya Kilimo..

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni siasa, siasa zetu hizi zipo kwenye kilimo, lakini kilimo ni amani, kilimo ni furaha, tukikosea kwenye kilimo, tumekosea uchumi. Kwa hiyo, tunahitaji kuwekeza sana kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bashe alikuja na Mpango wa Pili wa Maendeleeo ya Kilimo (Agricultural Sector Development Plan II). Baada ya ule wa kwanza ulioisha 2014, tukatengeneza mwingine ambao tunao, lakini bado tunaangalia contribution ya kilimo kwenye uchumi, it is only 3.9 percent.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kingine watu wengi wapo kwenye kilimo na Mheshimiwa Mwigulu anaposema anataka kukuza uchumi, hawezi kukuza uchumi kama anaacha hawa wakulima ambao ni more than 65 percent, hapo tutakuwa tunadanganyana, daktari wangu wa uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tu-invest kwa hawa 65 percent, tuta-invest vipi, niliwahi kuwasilisha hapa Bungeni, sekta ya umwagiliaji ndiyo sekta ambayo tunaweza tukawakomboa wananchi wetu. Tanzania ukiangalia, kuna matatizo makubwa sana, climate change, semi-arid and arid areas, haya yote hayawezi ku-predict kama tuna uwezo wa kuvuna au hautuwezi kuvuna. Mheshimiwa Mwigulu lazima awekeze kwenye sekta ya umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo makubwa matatu ambayo yanafanya sekta ya kilimo isiweze kuchangia vizuri kwenye pato la Taifa. Kwanza, tume-ignore sana sekta ya umwagiliaji. Nitaonyesha, Bajeti yetu 2019/2020, Serikali ilitenga only 32 billion (bilioni 32) kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji; mwaka 2020/2021 Serikali ilitenga only 12 billion (bilioni 12) kwa ajili ya shughuli za umwagiliaji. Mwaka 2021/2022, mama yetu akaongeza ikafika 46.5 billion kwenye sekta ndogo ya umwagiliaji. Mwaka huu, mama yetu akatupa bilioni 361.5 kwenye Sekta ndogo ya Umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nichukue fursa hii kumpongeza sana na kumshukuru sana Rais. Tumetoka 46 billion mpaka 361 billion kwenye Sekta ya Umwagiliaji. Mama yetu ana maono kwenye Sekta ya Kilimo kama nilivyotangulia kusema. Kama tuta-ignore Sekta ya Kilimo, tusitegemee uchumi wetu utakua kwa kiwango ambacho tunakitegemea, kwa hiyo lazima tuwekeze kwenye kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna mambo manne ambayo yanatusumbua. Jambo la kwanza financing hata hii 361 billion ambayo tumeiweka mwaka huu, ukiongea na wataalam wa irrigation wanakwambia kama tunataka kilimo chetu kweli kijikite kwenye umwagiliaji we need a minimum of 600 billion (bilioni 600) kwa mwaka. Lazima tuchukue maamuzi magumu, tuwekeze kwenye kilimo cha umwagiliaji. Tunahitaji a minimum 600 billion ili angalau tujikite kwenye umwagiliaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo moja katika umwagiliaji, tuna miradi mingi ya umwagiliaji, lakini traditional irrigation, inasubiri mvua, mvua isipokuja zile scheme zote zinakufa. We need to shift, lazima tuhame kutoka huko. Tunahitaji kujenga mabwawa, najua mwaka huu Mheshimiwa Bashe amekuja na plan ya kujenga mabwawa, we need to transform our agriculture, lazima tubadilike.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, tuna Tume ya Umwagiliaji, ukiangalia ile Tume, ipo Dodoma tu. Vile vile scope yake ni ndogo lazima tui-transform hii Tume. Nashauri upande wa Tume kwa nini tusi-transform iwe mamlaka. Nimepitia nchi nyingi, kwa mfano Kenya, Kenya wana National Irrigation Authority, Ghana wana National Development Irrigation Authority. Sasa sisi tuna katume kapo confined Dodoma, ukienda wilayani hukakuti, mkoani sijui ndiyo wana mtu mmoja na kadhalika, no, we need to shift. Kwa hiyo, nashauri hebu tuibadilishe hii tume yetu iwe na mamlaka kamili wawe na manpower. Tunahitaji kuona hii mitambo ipo located kule kwenye halmashauri zetu. Hiyo mitambo ya kujenga mabwawa, mitambo ya ku-repair hizo schemes zetu iwe kule, kuliko mtu anatoka Bukoba anakuja Dodoma kufuatilia mtambo uende ukafanye maintenance ya scheme iliyoko Bukoba. Kwa hiyo, niliona hilo ni eneo muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kama tunataka kubadilika kwenda kwenye kilimo cha umwagiliaji Serikali ni lazima iwekeze kwenye man power. Tunahitaji vijana ambao ni trained kwenye masuala ya irrigation system. Tunahitaji watu wa cheti na diploma, hawa ndiyo watakaofanya kazi na wakulima kule vijijini, hatuhitaji masters na degree kule vijijini, tunahitaji watu wenye certificate pia wale wenye diploma ambao wataweza kusaidia huku, hilo ni eneo jingine ambalo niliona nilishauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo niliona nishauri ni kwamba, ukiangalia scheme zetu nyingi zimechoka sana na nyingi zinategemea mvua kama nilivyosema, tunahitaji kujenga mabwawa. Hatuwezi kujenga mabwawa kwa bajeti ambayo tunaweka, hata hivyo tunamshukuru Mheshimiwa Rais ameliona hili mwaka huu ndiyo maana ame-shift bajeti from 46 Bilioni to 361 billion haijawahi kutokea, nine times. Kwa hiyo hilo ni eneo ambalo ninaomba bajeti ya mwaka huu Mheshimiwa Mwigulu, tunahitaji kuona bajeti angalau ni ya Bilioni 600. Tunataka watu wajikite kwenye kilimo cha umwagiliaji ili tuweze ku-transform kilimo chetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, pale Manyoni nina mradi wangu mmoja unaojulikana kama mradi kwa ajili ya ukaguzi wa magari wa pamoja. Mheshimiwa Mwigulu anaufahamu, ule mradi upo chini ya Wizara ya Fedha ulisimama tangu mwaka 2016. Sasa ninakuomba Mheshimiwa Mwigulu, hii ni miradi ya kimkakati ambayo inakuja kuchochea masuala ya uchumi. Hebu nalo liangalie ule mradi wa Muhalala ambao ulisimama pale tangu 2016, mradi wa zaidi ya Bilioni 35 na wenyewe tuufufue ili uweze ku-stimulate kwenye masuala ya uchumi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa hii nafasi, lakini kipekee nichukue nafasi hii nimshukuru sana Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, ndugu yangu Mheshimiwa Innocent pamoja na Naibu Mawaziri wote, lakini niungane na wenzangu waliotangulia kuwashukuru sana TARURA kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya. Wote ni mashahidi tangu TARURA imeanzishwa kuna mabadiliko makubwa sana kule vijijini kwenye barabara zetu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Rais. Sisi wananchi wa Jimbo la Manyoni Mashariki tunajivunia sana uwepo wake. Ndani ya mwaka mmoja tumepata fedha nyingi sana upande wa fedha za UVIKO, upande wa fedha za afya, lakini maeneo mbalimbali tumepata fedha nyingi sana. Kwa hiyo, tunamshukuru sana na tunaomba mtufikishie salamu hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nina hoja kubwa mbili. Hoja ya kwanza naomba nichangie kuhusu mfumo wa miradi ya kimkakati, nitatolea mfano kuhusu ujenzi wa stendi katika Halmashauri zetu,

lakini hoja ya pili ni kuhusu mfumo wa upandishaji hadhi Mamlaka ya Miji Midogo na nitatolea mfano wa Mamlaka ya Mji Mdogo Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nyote ni mashahidi kwamba, Halmashauri nyingi hazina stendi za kisasa za mabasi. Mfano mdogo ni Halmashauri yangu ya Manyoni, lakini Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Wizara ya Fedha wana mfumo unaitwa miradi ya kimkakati kwa ajili ya Halmashauri kuomba fedha kwa ajili ya hiyo miradi ya kimkakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huu mfumo una mapungufu mengi sana. Mojawapo ya pungufu la huu mfumo kwanza kuna Halmashauri nyingi ambazo hazina uwezo wa kujisimamia zenyewe ziandike yale maandiko, hazina uwezo wa kujisimamia zenyewe zifanye zile stadi kwa mfano environmental impact assessment, feasibility design, detail design, na kadhalika. Ili Halmashauri iweze kupata zile fedha lazima wakidhi vigezo nane na mojawapo ya kigezo ni kama hayo niliyoongea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi Halmashauri zetu hazina man power ya kutosha ya kuandika yale maandiko. Kwa Halmashauri zenye fedha zinahitaji zaidi ya milioni 300 ili kum-hire consultant ambaye atakuja kuandika hayo maandiko. Hili ni tatizo kubwa sana limesababisha Halmashauri nyingi mpaka sasa hivi zimeshindwa kutekeleza miradi ya kimkakati hususan stendi, ikiwepo Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni kwanza namshauri Waziri naomba pitia upya huu mfumo wa miradi ya kimkakati ili uzingatie Halmashauri ambazo zina mapato ya chini Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa mlishikilie hili. Pili, tuna taasisi zetu ambazo zina deal na masuala ya ujenzi, NSSF, PSSF, NHC kwanini tusiingienao ubia tukawapa wakajenga wakatuachia tukatumia tukawa tunarudishia kidogo kidogo? Lengo letu ni kuhakikisha tunakuwa na stendi ambazo zitakuwa chanzo cha mapato vilevile tuta-beautify Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni suala la mfumo wa upandishaji hadhi Mamlaka ya Mji Mdogo. Katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki nina Mamlaka ya Mji Mdogo ambayo iliundwa 2014. Mpaka sasa hivi nina miaka nane tangu Mamlaka ya Mji Mdogo Manyoni imeundwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukishaunda mamlaka ya Mji Mdogo unasimiwa na mtu anaitwa TownShip Executive Officer (TEO), lakini una-dissolve wale watendaji wa vijiji. Mpaka sasa hivi katika vitongoji 30 vinasimamiwa na Wenyeviti wa Vitongoji kwa zaidi ya miaka nane. Hili ni tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo ni kwamba, kwanza naungana na Wabunge wenzangu, Madiwani wetu wanafanya kazi kubwa sana, Wenyeviti wetu wanafanya kazi kubwa sana, lakini hawa kwa mfano kwenye Mamlaka ya Miji 30 hawana Watendaji wa Vijiji wenyewe wame-substitute role za Watendaji wa Vijiji. Hawa wanalipwa 40,000 kwa mwezi, lakini kwa sababu mapato yanasumbua wakati fulani wanakaa miezi Minne hadi Mitano hawajawahi kulipwa, hili ni tatizo kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kitu hapa, kwanza; niishauri Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa kama mnaona hii Mamlaka ya Miji Midogo mliyoianzisha haina tija ni vizuri mkaifanyia tathmini badala ya kukaa nayo miaka 10 hamjaipandisha hadhi. Kwa hiyo, niombe Mheshimiwa Waziri unda timu ifanye tathmini ya hii mamlaka ya Miji Midogo mliyoianzisha whether tunahitaji kuendelea nayo au hatuhitaji kuendelea nayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili. Kwa Halmashauri yetu ya Manyoni, kwenye Mji Mdogo wa Manyoni nimesema kwamba, ndani ya miaka nane tumekuwa tukiwatumia Wenyeviti wa Vitongoji kutekeleza miradi mikubwa ambayo Mama Samia anatuletea. Hili ni tatizo kubwa…

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Ally Mlaghila. Umesimama kwa Kanuni gani?

T A A R I F A

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni ya 77(1).

MWENYEKITI: Endelea.

MHE. ALLY A. J. M. JUMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwamba, huko kwenye Miji Midogo Madiwani wetu hata siyo tena Wenyeviti wa Kamati za Maendeleo kwa hiyo, wako pale kama vivuli. Ahsante.

MWENYEKITI: Ukitoa taarifa lazima Kiti kijiridhishe kwamba hii ni taarifa. Kwa hiyo, ni vizuri Waheshimiwa Wabunge tunapotoa taarifa tuipime sana. Mheshimiwa Spika ameshatoa mwongozo kuhusu aina ya taarifa hapa Bungeni.

Mheshimiwa endelea.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na ninaomba unilindie muda wangu. Nilichokuwa nikisema ni kwamba, naungana mkono na Waheshimiwa Wabunge ambao wamependekeza posho za Madiwani zibadilike ziwe mishahara lakini kwa upande wangu mimi naongezea suala la Wenyeviti wangu wa vitongoji vya Manyoni, Mamlaka ya Mji Mdogo wa Manyoni na Wenyeviti wa Vijiji vyote. Kwa Mamlaka ya Mji Mdogo wa Manyoni ndani ya miaka nane hawa wame-substitute role ya Watendaji wa Vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hatuna Watendaji wa Vijiji zaidi ya 30 katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Manyoni, hili ni tatizo kubwa. Kwa hiyo, ningeshauri Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa muangalie kama bado nafasi ya kupandisha hadhi mamlaka ya Mjhi Mdogo kuwa Halmashauri ya Mji ni vizuri sasa tukaongeza posho za hawa Wenyeviti wa vitongoji katika Mamlaka ya Mji Mdogo wa Manyoni. Hili tunaweza tukalifanya kwa nchi nzima, lengo letu ni kuhakikisha kwamba, tunawapa morali kusimamia miradi mbalimbali ambayo fedha tunapewa na Mama Samia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya mimi naomba nirudie kusema namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya na wananchi wa Jimbo la Manyoni tunampongeza sana, tunamuunga mkono na ninaomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa nafasi kuchangia kwenye Wizara nyeti, kipekee nimshukuru sana Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan kwa kazi ambayo anaendelea kuifanya hususan katika ku-promote utalii wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru sana Waziri wetu Mheshimiwa Jenista pamoja na ndugu yao Deo Ndejembi kwa Wizara ambayo wamepewa, hatuna mashaka kabisa na hawa wawili, Mheshimiwa Jenista tunamfahamu, tunafahamu utendaji wako tunaamini kabisa upele umepata mkunaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hoja kubwa mbili, hoja ya kwanza nataka nitoe uhalisia wa upungufu wa watumishi na nita-site mfano wa Manyoni DC, hoja ya pili vilevile nitoe ushauri kwa Serikali juu ya maboresho ya ile program yetu ya ya Maboresho ya Utumishi wa Umma (Public Services Reform Program). (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wenzangu wote wamesema kwamba tunao upungufu mkubwa sana wa Watumishi wa Umma kwenye kada mbalimbali. Nitatolea mfano kwenye Halmashauri yangu ya Manyoni, kwa upande wa Manyoni upande wa walimu wa shule za msingi, tunao upungufu wa zaidi ya asilimia 60 hadi sasa na ukizingatia tunazo shule 20 mpya za UVIKO ambazo zimejengwa nadhani hili Waziri wa TAMISEMI atakuwa amelichukua, kwamba kuna shule mpya ambazo Mama Samia ametujengea mpya ambazo tunategemea mwakani zianze kufanya kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Manyoni upande wa shule za msingi tuna zaidi ya upungufu wa asilimia 60 wa walimu wa shule za msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa Sekondari tuna upungufu wa zaidi ya asilimia 33 wa Walimu wa Shule za Sekondari. Jambo la kusikitisha ajira zilizotoka mwaka juzi au mwaka jana, tulipata walimu 11 tu ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, nadhani utaona sasa tuna upungufu wa zaidi ya Walimu 600 lakini rate ya kuajiri ni Walimu 11.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tuna very serious problem upande wa watendaji wa vijiji kati ya vijiji 58 nilivyonavyo ni vijiji 39 ambayo ni sawa na asilimia 67 vina Watendaji wa Vijiji. Tuna Vijiji 19 ambavyo vimekaa zaidi ya miezi Sita ambayo ni sawa sawa asilimia 33 havina Watendaji wa Vijiji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii maana yake ni nini? Mama Samia amepeleka fedha nyingi sana za miradi vijijini, tunategemea hawa Watendaji wa Vijiji ndiyo wasimamie hii miradi, hatuna watendaji wa vijiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, upande wa afya tuna upungufu zaidi ya asilimia 60 ya watumishi wa afya, (Human Resource for Health), hili ni tatizo kubwa na waliopo ni kama asilimia 38.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu upande wa utumishi ni kwanza, nadhani tunahitaji kuhuhisha mfumo wa ajira za Watendaji wa Vijiji. Huko nyuma Watendaji wa Vijiji wengi walikuwa wanatoka kwenye maeneo husika sasa hivi tunamchukua Mtendaji wa Vijiji Kigoma anakwenda kufanya kazi Bagamoyo, ndiyo ndugu yangu Mheshimiwa Tabasamu ameeleza pale. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri Mheshimiwa Waziri uangalie upya, kama inawezekana Watendaji wa Vijiji watoke kwenye maeneo ya karibu na ile halmashauri husika. Hii itapunguza hulka ya Watendaji wa Kijiji kuhama pia tuta- improve retention.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu utoaji wa vibali mbadala replacement. Wakati Waziri anakuja ku- windup nitapenda kujua standard operating procedure ukomo, hivi kwa mfano, samahani labda mtumishi amefariki replacement yake inatakiwa ichukue muda gani policy maxmum ni vizuri tukalijua hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ni kuhusu ile program yetu ya kuboresha utumishi wa umma. Tulikuwa na program nzuri sana ilianza 2002 awamu ya kwanza, ikaenda 2007 awamu ya pili, kutoka 2007 ikenda 2012 ikaisha, kuna maboresho makubwa sana yalifanyika katika utumishi wa umma. Swali langu la msingi ile program tangu ife nini mpango wa Serikali kuja na uendelevu wa Interventions ambazo zilifanywa na program ya kwanza na ya pili? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna wadau mbalimbali ambao wamekuwa na interest kubwa sana ya kusaidia Serikali, wakiwemo World Bank, USAID, GIZ, EU na wengine, ni nini mkakakati wa Serikali wa kuwa-engaged hawa wadau ili tuje na a new program ambayo itasaidia kuendeleza intervention za program one na program two.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haya ni maeneo nyeti sana, tumeona ripoti ya CAG bado kunachangomoto nyingi sana kwenye utumishi wa umma. Suala la accountability lakini kuna suala la ethical issues, suala la utendaji, suala la performance management, haya mambo yanahitaji kuboreshwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kila siku kuna uteuzi unaendelea, kwenye upande wa leadership viongozi wanatakiwa wanolewe, hii program ndiyo itakuwa muarobaini wa kuboresha utumishi wetu na utumishi wa umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya nakushukuru na ninaunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua nafasi hii kukushukuru wewe kwa kunipa hii nafasi, lakini kipekee nichukue nafasi hii nimshukuru Profesa Mkenda, Waziri wetu wa Elimu pamoja na Naibu Waziri wa Elimu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina hoja kubwa mbili ambazo nataka nimshauri Profesa pamoja na timu yake. Hoja yangu ya kwanza itajikita kwenye entry qualification za foreign students, naomba niongee Kiingereza; Vigezo vya kuwapata vijana wanaotoka nchi za nje kuja kusoma Tanzania. La pili nitaongelea ile foundation programme ambayo inatolewa na Chuo Kikuu Huria cha Tanzania tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze na suala la kwanza. Kwa upande wa admission ya foreign students vijana wanaotoka nje Kenya, Uganda, Zimbabwe na Malawi wanataka kuja kusoma Tanzania, bado tuna tatizo kubwa sana. Hili tatizo niseme limesababishwa na huu Mwongozo wa TCU, huu mwongozo wa TCU ambao ni third addition unasomeka end for standard and guidelines for university education Tanzania una kasoro nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nizieleze. Kasoro ya kwanza, wenzetu wa Kenya mfumo wao wa elimu ni 8, 4, 3 kwa Tanzania mfumo wetu wa elimu ni 7, 4, 2, 3, miaka saba shule ya msingi, miaka minne kidato cha nne, miaka miwili kidato cha sita, miaka mitatu na kuendelea Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wakenya wenyewe ni miaka nane shule ya msingi, miaka minne sekondari na kidato cha kwanza mpaka cha nne, miaka mitatu Chuo Kikuu hawana kidato cha tano, tatizo ni nini? Kijana ambaye amemaliza form four Kenya anaweza ku-accelerate kwenda kusoma Chuo Kikuu lakini ukimleta Tanzania haruhusiwi kusoma Chuo Kikuu, tuna tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kijana ambaye ametoka kwa mfano Uganda amesoma diploma, akija huku Tanzania hawezi kwenda kusoma mpaka watu wa TCU na NACTE wamfanyie equivalence, ili aweze kusoma.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ni nini hapa? Kwanza, ili vyuo vyetu viwe na international standard, hawa TCU wame-set a minimum standard of five percent enrolment ya foreign student kwenye vyuo vyetu, bila kuwa na a minimum five percent ya kuwa na idadi ya wanafunzi wanaotoka nchi za nje ndio hapo unajikuta chuo chetu labda cha Tanzania kipo 300 na ngapi, 2,000 na ngapi kidunia, hilo ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana nyingine ni kwamba, kumbe kuwa na idadi kubwa ya vijana wanaotoka nchi za nje kusoma Tanzania kunaongeza ubora wa elimu yetu na utambuzi wa elimu yetu kimataifa. Kwa maana hiyo ni kwamba tunapokuwa na vijana wengi wanatoka nchi za nje Kenya, Uganda Somalia Sudan Uingereza, wanakuja ku- improve diversity, vijana wetu watajifunza mambo mengi kutoka kwao. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa hivi kwa Tanzania idadi ya wanafunzi wa kutoka nchi za nje ni chini ya asilimia moja. hili ni tatizo kubwa sana. Kuna kitu kinaitwa education tourism, hawa vijana wakitoka Kenya, Uganda na Marekani, wakija Tanzania kusoma hawataishia kukaa UDOM tu, UDSM, SUA, au Mzumbe, watataka kutembelea mbuga zetu za Wanyama, tuna tatizo kubwa sana Profesa.

Mheshimiwa Naibu Spika, hoja yangu ya pili ni kuhusu hii foundation program. Kwa NACTE na TCU wame-set standards kwamba ili uweze kusoma Chuo Kikuu, kama ulikuwa umemaliza diploma lazima uwe na a minimum at least 3.0 GPA, kwamba kama una GPA chini ya 3.0, huwezi kwenda kusoma Chuo Kikuu kwa mtu mwenye diploma . Sasa kuna double standard, wakaruhusu Open University ndio wana-offer foundation program kwa wale ambao wameshindwa kukidhi GPA ya 3.0 hili waweze ku-accelerate kusoma degree na hiyo foundation program inatolewa mwaka mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, vyuo vingine havijapewa ruhusu ya kutoa foundation program, ni tatizo. Natoa mfano, Chuo cha Mipango, mwanafunzi amesoma pale mambo ya mipango ya maendeleo vijijini amepata GPA ya 2.5, anatamani aendelee kusoma degree ya mambo ya maendeleo vijijini, Open University hawana degree ya mambo ya rural development planning, unamlazimisha mtoto a-change kutoka professional yake kutoka rural development planning akasome professional nyingine, hilo ni tatizo.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo tuna tatizo ambapo tuna chuo kimoja tu Tanzania ambacho kinatoa foundation program kwa wale ambao hawana vigezo vya kusoma degree ili waweze kusoma degree. Ushauri wangu ni nini? Naomba niishauri Serikali na Wizara mambo matatu. La kwanza…

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, taarifa.

NAIBU SPIKA: Taarifa.

T A A R I F A

MHE. SOUD MOHAMMED JUMAH: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kumpa taarifa mchangiaji kwamba, mwaka jana kuna vijana wetu walikuwa wanatoka Chuo Kikuu cha Kampala wakapata ajali na hawa vijana waliopata ajali ni hawa vijana ambao hawana sifa ya kujiunga kutokana na haya masharti ya TCU, lakini wanakubalika nchini Uganda. Kwa hiyo tumepoteza maisha na vijana wengine vilema kwa sababu kubwa TCU wamewakwamisha kuweza kudahiliwa katika Vyuo Vikuu vya Tanzania na matokeo yake wakaenda Uganda na kwa vile safari ni ndefu ndio wakapata usumbufu. Ahsante sana.

NAIBU SPIKA: Dkt. Chaya.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakubali mchango na taarifa ya ndugu yangu Soud na naiunga mkono.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nishauri Serikali, kabla sijaishauri Serikali mimi ni mdau wa elimu, kwa hiyo naifahamu vizuri Wizara ya Elimu. La kwanza kuhusu foundation program, naomba itolewe kwa vyuo vyote na nina sababu za msingi. Sababu ya kwanza ni kwamba kwa Open University tayari wameelemewa ku-offer foundation program kwa vijana wote ambao wana GPA ya less than 3.0, naomba Wizara iruhusu SUA watoe foundation program, Mzumbe watoe foundation program, UDOM watoe foundation program, ili tuweze kuwapa nafasi vijana wengi wenye GPA ya chini ya tatu, waweze kusoma mwaka mmoja ili wa-move kwenye degree level. Hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, kuhusu hizi standards tofauti tofauti za elimu, sisi ni washiriki wa East African Community, lakini ni member wa SADC, niishauri Serikali, tunahitaji ku-harmonize education framework zetu za hizi nchi. Nimesema hapa Kenya wana mfumo wao tofauti wa elimu, Uganda wana mfumo tofauti wa elimu, Sudani wana mfumo tofauti wa elimu, Rwanda vilevile, tunahitaji sisi kama East African Community Block, tuwe na mfumo mmoja ili tuhakikishe kwamba tunatumia hii fursa vizuri ya kuchukua hawa vijana kutoka katika maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, la mwisho, ni suala la kutambua hizi entry qualifications. Kama alivyotangulia kusema ndugu yangu Mheshimiwa Soud kama kijana aliyemaliza form four Kenya, Wakenya wanamruhusu kusoma degree ni kigezo gani tumekitumia sisi Watanzania kumkataa yule aliyemaliza form four Kenya kusoma degree Tanzania. Hivi tukilinganisha Vyuo Vya Kenya na Vyuo Vya Tanzania kwenye international standard, vyuo vipi vitakuwa kwenye hadhi ya juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo naomba nimshauri Mheshimiwa Waziri lakini na Profesa wa TCU, wafanye utafiti wa kina ili waangalie kwa sababu hawa wanakuja kusoma Tanzania, at the end of the day wanarudi kufanya kazi kwao Kenya. Kwa hiyo sioni sababu ya kuwakataa hawa watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nakushukuru kwa kunipa hii nafasi. Kipekee namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya. Sisi katika Jimbo letu la Manyoni Mashariki kuna kazi nyingi sana zimeshafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki tumepata fedha nyingi sana. Tumepata shilingi bilioni nne kwa ajili ya ujenzi wa shule ya wasichana ya Mkoa; tumepata shilingi bilioni 1.4 kwa ajili ya ujenzi wa Chuo cha VETA; tumepata shilingi bilioni 12 kwa ajili ya mradi wa maji wa Kintinku Msilile; na pia tulipata shilingi bilioni 1.7 tukajenga shule tano mpya za sekondari. Haya ni mafanikio makubwa sana. Nasi watu wa Manyoni kwa kweli hatujawahi kupata fedha nyingi hizi huko nyuma, kwa hiyo, tunampongeza sana Mheshimiwa Rais na tunamtia moyo aendelee kuchapa kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimpongeze sana Waziri Mkuu na timu yake; Mheshimiwa Prof. Ndalichako na mama yangu pale, wanafanya kazi kubwa sana. Wanaitendea haki sana Wizara ya Waziri Mkuu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi leo nachangia upande wa ajira, lakini nataka nioneshe uhusiano uliopo kati ya ajira na ile taasisi yetu ya TAESA (Tanzania Employment Service Agency). Mheshimiwa Hasunga ameeleza hapa kwamba, tatizo la ajira Tanzania bado linaendelea kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikwambie, it is a time bomb. Ni bomu! Kwa sababu gani? Kwa mwaka, takwimu zinatuonesha, tunatoa vijana takribani 800,000 hadi 1,000,000 wanaingia kwenye soko la ajira, lakini ni chini ya asilimia 20 ya vijana wanapata ajira. Hili ni tatizo kubwa sana. Mimi nimefundisha katika taasisi za elimu ya juu, nina vijana ambao wamekaa zaidi ya miaka 10 tangu wamalize hawajapata ajira, wapo mtaani. Hili ni tatizo kubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tulianzisha TAESA 2002. Lengo la TAESA lilikuwa kuratibu ajira, lakini tujiulize, wangapi wanaijua TAESA? Je, TAESA ina capacity ya kuratibu tatizo la ajira? Vile vile tulianzisha TAESA ili iweze kuwa-connect wanaotafuta kazi na waajiri kwenye sekta binafsi na sekta ya umma. Je, haya yanafanyika?

Mheshimiwa Naibu Spika, TAESA iko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu. Mwaka 2016 walianzisha program ya mafunzo ya kazi kwa vijana wanaomaliza vyuo vikuu, inaitwa internship program; lakini mwaka 2017 Ofisi ya Waziri Mkuu ilianzisha Mwongozo wa Mafunzo ya Kazi kwa Vijana Wanaomaliza Vyuo Vikuu (National Internship Guideline).

Mheshimiwa Naibu Spika, tuna Mwongozo, lakini leo hii umewasikia Wabunge wengi wakisema, huko kwenye Halmashauri zetu kuna vijana wanachukuliwa wanajitolea, wanalipwa kiasi ambacho hakipo kwenye mwongozo. Nini maana ya kuanzisha huu Mwongozo ambao uko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu, ambapo tulitegemea utasaidia kuhakikisha kwamba, unaratibu suala la kutumia hata hawa vijana kwa part time, na vilevile kuhakikisha kwamba taasisi zote za umma na sekta binafsi wanatumia huo Mwongozo kwa ajili ya kuwasaidia vijana wetu?

Mheshimiwa Naibu Spika, program ya kuwapa mafunzo vijana waliohitimu vyuo vikuu hadi sasa takwimu nilizonazo, imefikia vijana zaidi ya 13,000. Hao vijana wanaingia mkataba wa miezi sita hadi 12, wanalipwa 150,000/= kwa mwezi. Maana yake ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, mpaka sasa hivi takribani shilingi bilioni 18 zimetumika kwa ajili ya hii programu. Swali langu linakuja, kuna uhusiano gani kati ya TAESA na Sekretarieti ya Ajira? Kuna uhusiano gani uliopo kati ya TAESA ambayo inawatafutia vijana ajira na Sekretarieti ya Ajira? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Sekretarieti ya Ajira imejikita kwenye ajira za umma. Sasa swali langu linakuja? Je, wale vijana ambao TAESA imewapa mafunzo, ni jinsi gani inaratibu kuhakikisha kwamba wale vijana wanaotoka TAESA inawapeleka kwenye Sekretarieti ya Ajira ili waweze kupata ile ajira?

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo. Hakuna link iliyopo kati ya TAESA na Sekretarieti ya Ajira. Hawa ni watoto wa baba mmoja na mama tofauti. Nilitegemea kwa sababu, TAESA ime-invest hela nyingi sana kuwajengea uwezo hawa vijana, nilitegemea zinapotoka ajira za Sekretarieti ya Ajira, kipaumbele kiwe kwa wale vijana waliotoka TAESA. Leo nikimwuliza Mheshimiwa Waziri aniambie ni vijana wangapi waliopata mafunzo ya TAESA, walipata ajira za Sekretarieti ya Ajira, inawezekana wakawa wachache sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna tatizo na kwa kweli, tunahitaji kulifanyia kazi. Tukiangalia katika nchi za wenzetu, kwa mfano Kenya. Kenya wana TAESA kama ya kwetu, lakini wenzetu walichofanya wameanzisha kitu kinaitwa National Employment Authority. Ukiangalia majukumu yake ni tofauti sana na ya kwetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, TAESA yetu haina meno. Tunategemea TAESA yenye meno ambayo itasaidia vijana wetu kupata ajira. Siyo lazima ajira ya Serikalini, lakini iweze ku-connect vijana wetu na ajira mbalimbali; iwatafutie ajira; iwajengee uwezo; na mambo mengine, lakini bado tuna tatizo kubwa sana kwenye suala la ajira.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali, kama nilivyotangulia kusema, tatizo la ajira bado ni kubwa sana. Kweli tunasema vijana wajiajiri, lakini mzazi anapopeleka mtoto shule, chuo, anategemea yule mtoto aje awe afisa; hayo ndiyo mategemeo ya kila mtu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa ushauri wangu ni nini? Kwanza, tunahitaji kupitia upya TaESA, tuipe nguvu ya kifedha, tunahitaji tufikie vijana wengi. Tuone uhusiano uliopo kati ya TaESA na Sekretarieti ya Ajira. Wale vijana ambao wamekuwa groomed na TaESA tunategemea wachukuliwe na Sekretarieti ya ajira; hilo la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, hizi taarifa za hizi nafasi za internship tunahitaji ziwe za uwazi. Vijana wote wa Kitanzania wapate. Nilitegemea kusikia vijana wangu wanaotoka Manyoni vilevile wamenufaika na huu mradi wa TaESA, lakini nikiuliza inawezekana nisiwapate.

Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu, nilitegemea kuona kuna kanzidata (database) ya kuhakikisha kwamba vijana wote wanaomaliza vyuo vikuu wanajiunga kwenye ile kanzidata ambayo itakuwa chini ya TaESA ili iwe rahisi TaESA wenyewe kuratibu masuala ya kazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nirudie kuishukuru sana Serikali, hususan Mheshimiwa Rais, kwa kazi kubwa mnayoifanya, sisi Manyoni ametupa miradi mingi sana. baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja; ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na nikupongeze sana kwa kuweza kusimamia Bunge letu kikamilifu kabisa. Pia nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa Manyoni sisi ametuletea fedha nyingi sana. Vilevile nimshukuru Waziri Kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene, lakini vile vile Naibu Waziri Ndugu yangu, Mheshimiwa Ridhiwani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nina maeneo matatu ningependa kuchangia. Eneo la kwanza linahusu upungufu wa Maaskari na hali ya usalama Manyoni, eneo la pili linahusu upungufu wa watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni na muda ukiniruhusu nitachangia kuhusu Standing Orders (Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma).

Mheshimiwa Spika, tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi hususani Maaskari katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni na katika Wilaya ya Manyoni. Vile vile, sanjali na hilo, Manyoni kumekuwa na matukio mengi sana ya uhalifu. Tangu 2017 kumekuwa na matukio ya aina tatu ya uhalifu. La kwanza, kumekuwa na matukio ya mauaji, watu wanauawa wanatupwa pale Manyoni Mjini. Pili, kumekuwa na tabia ya kufukua makaburi na kuchukua viungo na vitu mbalimbali. Hali hii imekithiri tangu 2017 tumekuwa na haya matukio.

Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kumshukuru sana RPC wa Mkoa wa Singida na Mkuu wa Mkoa wa Singida, lakini vile vile niishukuru Serikali, hivi karibuni imetuletea Mkuu wa Wilaya mpya Mheshimiwa Kemilembe. Wiki iliyopita Waziri wa Mambo ya Ndani amefanya mabadiliko pale Manyoni, ametuletea OCD mpya na amefanya mabadiliko ya Mpelelezi wa Wilaya.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba, tunahitaji sasa Serikali ituongezee watumishi wa Polisi lakini vile vile iangalie kwa ukaribu hali ya usalama wa Manyoni. Wastani kila mwezi mtu mmoja anaokotwa amekufa pale Manyoni Mjini, lakini watu wanafukua makaburi. Siku hizi wananchi wa Manyoni wanalinda makaburi, tukishazika inabidi uweke mlinzi kwa sababu ndani ya siku tatu unakuta makaburi yameshafukuliwa. Kwa hiyo, naomba tuliwezeshe Jeshi la Polisi, wana upungufu wa magari, hawana pikipiki na wana upungufu wa zaidi ya watumishi 10 pale Manyoni. Pia niombe wapeleke timu ikachunguze yale mauaji, kwa nini yale mauaji yanatokea pale Manyoni?

Mheshimiwa Spika, suala la pili, ni suala la upungufu wa watumishi pale Manyoni. Katika Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni, tuna upungufu mkubwa sana wa watumishi. Upande wa Afya mahitaji ni watumishi 642, lakini waliopo ni 289 na upungufu ni 353. Mgao wa mwaka jana tulipata watumishi wa afya 33 tu. TAMISEMI wametoa tangazo la kuajiri watumishi, tunaomba na kwa kupitia Waziri wa Utumishi, Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni tuangaliwe.

Mheshimiwa Spika, upande wa Walimu mahitaji upande wa sekondari ni 460, waliopo ni 268, upungufu ni takribani 138. Vivyo hivyo hata upande wa shule za msingi. Vilevile kwenye kada zingine, upande wa Uhasibu tuna upungufu mkubwa sana pale tuna Wahasibu watatu tu. Kati ya hao ni Mweka Hazina tu ndio ana CPA, lakini wengine wote hawana CPA. Nimeona hilo nalo niliombe na nimwombe kaka yangu Mheshimiwa Simbachawene na Mheshimiwa Naibu Waziri watusaidie tupate watumishi pale Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Spika, upande wa Walimu, mahitaji upande wa Sekondari ni 460 lakini vilevile waliopo ni 268 upungufu ni takribani 138. Vivyo hivyo hata upande wa shule za msingi. Vilevile kada zingine upande wa Uhasibu tuna upungufu mkubwa sana pale, tuna Wahasibu Watatu tu na kati ya hao ni Mwekahazina tu ndiyo ana CPA lakini wengine wote hawana CPA, nimeona hilo nalo niliombe na nimuombe Kaka yangu Simbachawene na Mheshimiwa Naibu Waziri mtusaidie tupate watumishi pale Halmashauri ya Wilaya ya Manyoni.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la wanaokaimu. Halmashuri ya Wilya ya Manyoni haina Mkurugenzi tangu mwaka jana mwezi wa Nane, tunae anaekaimu. Nilisikia wenzangu wakichangia hapa kanuni ya kukaimu, mtu anakaimu zaidi ya miezi Saba miezi Nane, kwa hiyo niliona nalo hilo tulione pia Wakuu wengi wa Vitengo wanakaimu, kwa hiyo hilo nalo niliona nilichangie.

Mheshimiwa Spika, jambo la mwisho naomba nichangie upande wa Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma. Katika Kanuni za Kudumu za Utumishi wa Umma kuna maeneo matatu ningependa kuchangia. Eneo la kwanza kuhusu wazazi tunapofiwa sisi na wazazi watumishi wa umma, wazazi hawawi considered kwenye suala la mazishi, lakini mnajua msiba unapotokea wa mzazi tegemeo kubwa ni kwa mtumishi. Ningeomba Mheshimiwa Waziri hebu liangalieni hili, wazazi wawe considered kwenye suala la kuwahudumia kwenye mazishi, baba, mama anapofariki. Kwa kweli, huwa watumishi wetu wanapata shida sana inapotokea msiba wa mzazi, anaanza kuhangaika kukopa na kadhalika, kwa hiyo hili ni eneo la kwanza ambalo nilidhani ni eneo ambalo tunahitaji kubadilisha zile standing order zetu tuweze kuwa- accommodate wazazi.

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la mtu kuwa Mkuu wa Idara, taarifa ya CAG inaonesha kwamba maeneo mengi Wakuu wa Idara wanakaimu, wanakaimu kwa sababu ya vigezo vyetu vya mtu kuwa Mkuu wa Idara. Ili mtu awe Mkuu wa Idara anatakiwa awe Afisa Mwandamizi, sasa hicho ni kigezo cha juu sana, lakini huko nyuma tulikaa muda mrefu watu hawajapata promotion.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni nini? nadhani tungeangalia maeneo kwa mfano, kuna kada ambazo ni ngumu sana kupata watu wenye kuwa Waandamizi kwa mfano TEHAMA, Sheria, Manunuzi, hawa watu tuwachukue hata wale wa Grade One ili angalau wawe Wakuu wa Idara nadhani hilo litasaidia sana kuhakikisha kwamba tunakuwa na Wakuu wa Idara ambao wanakidhi vigezo lakini vilevile tutajibu ile hoja ya CAG.

Mheshimiwa Spika, lingine suala la likizo ya uzazi. Katika likizo ya uzazi kuna mambo matatu ningependa kuchangia, kwanza ni pale mama anapojifungua halafu bahati mbaya mtoto akafariki. Standing order inampa siku 42 za kupumzika, lakini jamani siku 42 ni siku chache sana, mama anapojifungua mtoto akafariki bado anakuwa na machungu mengi, mnataka ndani ya siku 42 arudi tena kazini, mimi ningeshauri hata wale mama ambao wanajifungua mtoto anafariki wapewe zilezile siku 84 kwa sababu anakuwa bado anapitia mazingira magumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la tatu ni kuhusu wanaume, mama amejifungua standing order inasema inampa siku tatu, mama amejifungua kwa operation, siku tatu mwanaume ndiyo anatakiwa amhudumie then aendelee na kazi zingine, nadhani hapa kuna tatizo vilevile kwa hiyo nishauri na yenyewe muiangalie na ningependekeza angalau basi na baba apewe angalau siku Saba ili apate muda mzuri wa ku- take care mke wake wakati huo anauguza vidonda vya operation. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la mamlaka ya nidhamu katika Halmashauri zetu kuna mkanganyiko. Kanuni zilizorekebishwa zinasema mamlaka ya nidhamu ni Mkurugenzi lakini sheria inasema mamlaka ya nidhamu ni Baraza la Madiwani. Sasa hapa ningeshauri iangaliwe hii kama tumeamua mamlaka ya nidhamu katika Halmashauri zetu awe Mkurugenzi kote isomeke Mkurugenzi, lakini kama tunasema mamlaka ya nidhamu katika Halmashauri zetu wawe Madiwani basi kote kuwe Madiwani.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya nakushukuru sana na naunga mkono hoja, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Madini
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi nashukua nafasi hii kukushukuru wewe kunipa hii nafasi ya kuchangia kwenye bajeti ya Wizara ya Madini. Kipekee ninamshukuru sana Rais wetu Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa ambayo anaendelea kuifanya katika Taifa letu la Tanzania, namshukuru Ndugu yangu mtani wangu, Waziri wa Madini Dkt. Biteko na Kaka yangu pale Naibu Waziri wa Madini Dkt. Kiruswa. Pia ninampongeza na kumshukuru Afisa Madini wa Mkoa wa Singida kwa ushirikiano mkubwa ambao anaendela kutupatia watu wa Singida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nitaongelea mambo mawili jambo la kwanza nitaongelea fursa ya madini ya dhahabu - Manyoni lakini jambo la pili nitaongelea fursa ya madini ya chumvi - Manyoni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza na fursa ya madini ya dhahabu Manyoni. Mika miwili iliyopita Rais wetu wakati akiwaapisha Makatibu Wakuu kama sijakosea aliwahi kutamka na alitoa challenge kwa Wizara mbili, Wizara ya Madini na Wizara ya Maliasili aliwaambia kuna baadhi ya mapori ya akiba na hifadhi yanasemekana kwamba yana madini, lakini inaonekana hakuna jitihada zozote zile za kuhakikisha yale madini yanachimbwa, na akasema kwamba hivi wale Tembo na Digidigi watakula hayo madini, hizo dhahabu? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki na katika Wilaya ya Manyoni tuna mapori ya akiba matatu, tuna Pori la Akiba la Kizigo, tuna Pori la Akiba la Muhesi na tuna Pori la Akiba la Rungwa. Katika haya mapori yote matatu kuna viashiria vya madini. Huko nyuma iliwahi kutokea booming ya madini ya dhahabu katika Kata ya Sasilo, eneo linajulikana Iruma ambako kuna Pori la Akiba la Muhesi na Kizigo. Vilevile katika Kata ya ya Rungwa, Kata ya Mwamagembe kuna madini ya dhahabu na kule nako kuna pori la akiba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Kata ya Iseke Kijiji cha Simbangulu kuna eneo linaitwa Myunga, hili ni eneo mabalo ni very popular kwa watu wanotoka Kata ya Isseke, kila nikienda kufanya mikutano kwanza wananchi wanalalamika sana, kila wakati wanafukuzwa na watu wa Maliasili, kule kunasemekana vilevile kuna viashiria vya madini ya dhahabu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi sasa kwenye ile kauli aliyoitoa Rais wetu Mama Samia Suluhu Hassan, aliwapa challenge hizi Wizara mbili waende wakatafakari watuambie, kwa nini kama kuna maeneo ambayo yana madini ni Hifadhi za Taifa au Mapori ya Akiba, kwa nini tusije na utaratibu rafiki wa kuhakikisha kwamba tunakuwa it is a win-win situation, wafanye cost benefit analysis, watuambie hivi tukisogeza mpaka tukachimba madini, je italeta athari kwenye hizo hifadhi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ni nini? Ningemshauri Waziri wa Madini na Waziri wa Maliasili na Utalii watuletee taarifa kutokana na kauli aliyoitoa Rais mmeifikia wapi, hatujaona utekelezaji wa agizo la Rais. Rais akishatamka ni agizo lakini mpaka leo hii tukienda kwenye mikutano watu wanauliza mbona Rais alishauri, aliagiza hatuoni utekelezaji? Kwa hiyo, nawashauri hawa ndugu zangu wawili Waziri wa Madini na Waziri wa Maliasili na Utalii hebu nendeni mkalichakate hili, mtuambie kama kuna potentiality ya sisi kuchimba yale madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingene sanjari na hili ukiangalia kwa mfano yale mapori ya akiba ukiangalia michango yao hata kwenye ile service levy ya Halmashauri ni ndogo sana, kwa mwaka sijuwanachangia Milioni 30 tu, sasa ukiangalia contribution yake is almost insignificant. Kwa hiyo, mimi ningeshauri kwa kweli tuangalie kama hayo maeneo tunaweza tukawachia wenzetu wa madini, wakachimba na yakawa na impact kubwa kwenye GDP lakini yakawa na impact kubwa kwenye mapato ya ndani ya Halmashauri mimi ningeweza kushauri hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine tuna madini eneo linaitwa Londoni ya dhahabu, ndugu yangu mtani wango Dotto unayafahamu. Ndugu yangu Dotto wewe ni mtani wangu siyo ndugu yangu, pale kinachokosekana ni umeme tu, ukipeleka tu umeme utaongeza kiwango cha uchimbaji wa madini pale Londoni Makulu. Kwa hiyo ninaomba mtani wangu Mheshimiwa Dotto hebu nisaidie hili, wapelekee umeme wale wachimbaji wadogowadogo pale Londoni ili tuongeze uchimbaji wa madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho na la pili ni fursa ya madini ya chumvi. Leo nilipitia madukani nimekutana na chumvi inatoka India, nimekutana na chumvi inatoka Kenya, Mheshimiwa Halamga hapa ameeleza tuna-deposit za chumvi nyingi sana Tanzania, tuna kiwanda cha chumvi Kigoma, tuna kiwanda cha chumvi Tanga na Dar es Salaam. Tuna chumvi Lindi, Simiyu na Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Jimbo la Manyoni Mashariki kuna eneo linajulikana kama Kinangali na ile chumvi inajulikana kama chumvi ya Kinangali. Naibu Waziri ulishafika mwaka jana ninakushukuru sana, ulitembelea zile site zote tatu kuanzia Mahaka, Majiri, Kinangali na Mpandagani, ukaagiza Afisa Madini wa Mkoa wafanye utafiti, sasa mpaka sasa hivi taarifa ya utafiti siifahamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu ipo katika maeneo makubwa mawili, kwanza mimi tangu nizaliwe natumia chumvi ya Kinangali mpaka leo hii hakuna uwekezaji wowote wa Serikali katika eneo la Kinangali! Sasa najiuliza kama mimi tangu nizaliwe sasa hivi nakimbilia miaka 50 natumia hiyo chumvi, then utaniambia kwamba chumvi hakuna pale Kinangali hapana! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri Serikali watuambie Je, ni kwa kiwango gani ile chumvi ipo pale in terms of quantity, pili watuambie Je, ile chumvi ina ubora? Tatu watushauri sasa kwamba Je, tunaweza kuweka uwekezaji wa aina gani? Tunahitaji viwanda vya size ya kati, lakini viwanda vidogovidogo kwa ajili ya kuwasaidia ndugu zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nirudie kumshukuru sana Waziri wa Madini.

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Chaya kabla haujahitimisha naona kuna taarifa hapa, kutoka kwa Mheshimiwa Cecil Mwambe.

TAARIFA

MHE. CECIL D. MWAMBE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa Mheshimiwa Chaya kwamba kuna uzembe mkubwa sana ufanyika kwenye uwekezaji wa chumvi, ukiangalia eneo la Bahari toka Lindi mpaka Tanga eneo hili lote lina chumvi lakini bado wawekezaji wanaruhusiwa kuingiza chumvi nchini kitu ambacho siyo sahihi. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Dkt. Chaya unapokea taarifa.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napokea taarifa ya Mheshimiwa Cecil na labda kabla sijamalizia kama alivyotangulia kusema Mheshimiwa Cecil, sisi kama Nchi hatujawekeza vizuri kwenye fursa ya chumvi hususan katika eneo langu la Manyoni katika Kata ya Majiri hususan Kinangari. Nadhani ni fursa ambayo ingeweza kukuza ajira. Ile chumvi inachukuliwa na watu kutoka Congo, Rwanda na Burundi wanachukua kama raw material wanaenda ku-process wanai-process halafu wanaturudishia tunakuja kununua kwa bei ya jumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, nichukue nafasi hii kukushukuru kwa kunipa nafasi hii. Vilevile kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambazo anaendelea kuzifanya. Nimeongea mara nyingi hapa, sisi Manyoni Mashariki tumepata miradi mingi sana ikiwepo hii miradi ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile nichukue nafasi hii kumshukuru sana Waziri, ndugu yangu Mheshimiwa Bashe pamoja na Naibu Waziri, ndugu yangu na mdogo wangu Mheshimiwa Mavunde, kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, lakini bila kuwasahau watendaji wetu wa Wizara ya Kilimo hususan, Bodi ya Korosho, lakini Bodi ya Umwagiliaji na Katibu Mkuu. Mheshimiwa Bashe ametusaidia sana kwenye kilimo cha korosho Manyoni. Najua kuna mambo mengi ameyafanya, sasa hivi kilimo chetu cha korosho Manyoni kinaenda vizuri sana. Sasa hivi anajenga maghala, lakini ametupelekea pikipiki, lakini kuna vitu vingi sana ambavyo amevifanya kwa hiyo, namshukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo nina ajenda kubwa mbili ambazo ningependa kuchangia kwenye Wizara ya Kilimo. Eneo la kwanza nitachangia upande wa skimu za umwagiliaji na eneo la pili nataka niishauri Serikali jinsi gani tunaweza tuka-transform Tume ya Umwagiliaji. Wachangiaji wengi wameeleza hapa kuhusu umuhimu wa Tume ya Umwagiliaji kwa hiyo, naomba nichangie eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, upande wa skimu za umwagiliaji; kwanza nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri, alimtuma Naibu Waziri, Mheshimiwa Mavunde alikuja Manyoni pale Chikuyu kwenye Skimu ya Umwagiliaji wa Chikuyu. Ile skimu ilikaa miaka mitatu wananchi hawajalima, lakini alikuja akatoa maelekezo na nimshukuru sana Mkurugenzi wa Tume ya Umwagiliaji walikuja wakaikarabati ile Skimu ya Umwagiliaji ya Chikuyu, lakini bahati mbaya mwaka huu tena ule mto ukaenda kubomoa sehemu fulani ya ile skimu.

Mheshimiwa Spika, nimeona kwenye bajeti ya Waziri kwamba, ameweka vilevile kukarabati hii Skimu ya Chikuyu. Nimwombe tena Mheshimiwa Waziri, tukamalizie ile kero ili tuwape matumaini wakulima wa hapo chikuyu.

Mheshimiwa Spika, Tarafa ya Kintinku, Tarafa ya Bahi na Tarafa ya Kilimatinde sisi tunategemea kilimo cha mpunga na kilimo cha mpunga kinahitaji umwagiliaji. Nimeona kwenye bajeti ya kilimo wameweka ukarabati wa Skimu ya Ngaiti, Skimu ya Maweni, Skimu ya Lusilile, ya Udimaa hata ya Msemembo. Nimwombe sasa Waziri, ukarabati huu uende kufanyika, hawa wananchi asilimia 100 wanategemea kilimo cha umwagiliaji. Bila kuwepo miundombinu ya umwagiliaji ambayo ni mizuri maana yake tunatengeneza njaa kwa hawa watu.

Mheshimiwa Spika, nimwombe sana Mheshimiwa Waziri pamoja na mdogo wangu Mheshimiwa Mavunde wajitahidi wakawasaidie hawa ndugu zangu wa Ngaiti, Maweni, Mtiwe, Chikuyu, Msemembo, lakini Udimaa na Lusilile hizi skimu zao mwaka huu zikatengenezwe, zikakarabatiwe ili angalau mwaka unapoanza wa kilimo waweze kulima.

Mheshimiwa Spika, lingine, Waziri mwaka jana alikuja na bajeti ya kusema kwamba, anaenda kuanza kufanya feasibility study ya Mradi wa Bwawa la Mbwasa. Nimefurahi kwenye bajeti hii vilevile Waziri ameeleza hapa kwamba anaenda kufanya mapitio ya ile feasibility study ambayo ilishafanyika muda mrefu sana, lakini vilevile anaenda kuanza kujenga Bwawa la Umwagiliaji la huu Mradi wa Mbwasa.

Mheshimiwa Spika, huu mradi wananchi wameusubiri kwa muda mrefu sana. Nakumbuka Mheshimiwa Naibu Waziri Mavunde alipokuja wananchi walimuuliza na aliwaahidi kwamba, Serikali ipo mbioni kuhakikisha kwamba, huu mradi unaanza kujengwa. Kwa hiyo, nimwombe Mheshimiwa Waziri auchukue huu Mradi wa Umwagiliaji wa Mbwasa kwa sababu ni mradi ambao utawaokoa sana wananchi wa Manyoni, hususan Tarafa ya Kintinku ambako wanategemea zaidi kilimo cha umwagiliaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lingine, tuna bodi yetu ile Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, nilitegemea sasa tunapoongelea kilimo cha mpunga katika hizi tarafa tatu, Tarafa ya Bahi, Tarafa ya Kintinku na Kilimatinde, tuwe tuna uwekezaji wa masoko angalau katika hizi tarafa tatu. Hatuna masoko ya uhakika ya mpunga, tuna madalali tu na walanguzi ambao wanaingia kwenye eneo lile la Kintinku, Bahi na hata Kilimatinde.

Mheshimiwa Spika, nimwombe Waziri, tuna Bodi ya Nafaka na Mazao Mchanganyiko, awa-task hawa watu waweke miundombinu pale, maghala, lakini watuanzishie masoko ili wananchi wetu wawe na uhakika wanapouza mpunga wanauza kwa bei ambayo itakuwa na manufaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, la mwisho ni kuhusu hii Tume ya Umwagiliaji. Watu wengi wamechangia kuhusu hii Tume ya Umwagiliaji. Niseme kweli na nimekuwa nikichangia sana, hatuwezi kuendeleza kilimo cha Tanzania kama hatutawekeza kwenye hii Tume ya Umwagiliaji. Ni eneo ambalo kwa kweli, tunahitaji kuwekeza. Nimshukuru sana Mheshimiwa Rais mwaka huu, kuanzia Rais Dkt. Samia alipoingia madarakani bajeti ya Wizara ya Kilimo imepanda sana, mwaka jana ilikuwa bilioni 700, mwaka huu tuna bilioni zaidi ya 900, lakini vilevile bajeti ya umwagiliaji imepanda, mwaka jana tulikuwa na bilioni 262, mwaka huu tuna bilioni 373, haya ni mapinduzi makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji kufanya vitu viwili. Eneo la kwanza ambalo naliona na ningependa kushauri, kwa nini hii Tume yetu tusii-transform? Hapa ukisikiliza Wabunge wengi wameongelea suala la umwagiliaji, we need a giant institution, tunahitaji kuja na kitu tofauti na tume, kwa nini tusifikirie kuja na authority, National Irrigation Authority? Kama tulivyokuja na RUWASA, TARURA, TANROADS, iwe giant? Tuipe meno, tuipe fedha, ili iweze ku-manage suala la irrigation kwa Tanzania? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nilitegemea kwenye taarifa ya Mheshimiwa Waziri angeeleza kwamba, lini anakuja kuanzisha National Irrigation Authority ambayo sasa itaenda ku-spear head masuala ya umwagiliaji. La pili, tunapofikiria kuanzisha hii authority, lazima tufikirie kwenye financing frame work, fedha tutapata wapi? Ukiangalia kwa kiasi kikubwa vyanzo vya fedha vya hii tume ni zile tozo za wakulima kutoka kwenye skimu, skimu ambazo hatujazikarabati. Nashauri, tunahitaji kuja na mfumo mzuri wa kutafuta vyanzo vya mapato, mbona tunatoza maeneo mengine kwa nini tusitoze asilimia tatu kwa wakandarasi ile asilimia tatu ikaingia kwenye hiyo Tume ya Umwagiliaji? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kwa kweli katika haya Mheshimiwa Waziri, alichukue hili, hasa hasa la kwenye suala la ku-transform Tume ya Umwagiliaji. Sisi Wabunge wengi tunategemea kwamba, kama tuta-invest kwenye suala la irrigation, umwagiliaji, tunaweza kwenda ku-transform kilimo cha Watanzania, lakini kama tutakuwa hatuna uwezo wa kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji uwezo wa ku- transform kilimo utakuwa ni mdogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo nirudie tena kumshukuru sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri kwanza kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya, lakini nimshukuru sana Mwenyekiti wa Bodi ya Korosho, amefanya mambo makubwa sana Manyoni. Nimshukuru sana vilevile Mwenyekiti wa Bodi ya Mazao Mchanganyiko na Mkurugenzi kwa kazi kubwa ambayo anaifanya.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya naunga mkono hoja na nakushukuru sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Maji
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Spika, kipekee nikushukuru kwa kunipa hii nafasi ili nichangie kwenye Wizara ya Maji. Pia nichukue nafasi hii kipekee vilevile nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi nyingi ambazo anazifanya. Katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki tulikuwa na miradi mingi ya maji kichefuchefu, lakini nikwambie sasa hivi miradi mingi ya maji katika Jimbo la Manyoni Mashariki inaenda vizuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Aweso, ndugu yangu, lakini na Naibu Waziri, Mheshimiwa Engineer Mary. Wengi wamesema hapa hawa vijana wetu, ndugu zetu wanafanya kazi nzuri sana. Kwangu Mheshimiwa Aweso nadhani anaenda kuweka historia kubwa sana ya kutatua kero ya maji Manyoni. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna Mradi wa Kintinku - Lusilile na siku hizi unaniita mzee wa Kintinku - Lusilile. Huu mradi una miaka 15 ulishindikana kukamilika wa bilioni 12, lakini hapa ninapovyoongea mwezi uliopita mkandarasi alipewa bilioni mbili kwa ajili ya kwenda kukamilisha Mradi wa Kintinku - Lusilile. Nimwombe Mheshimiwa Waziri, huu mradi wa bilioni 12 ni mradi mkubwa sana, ukikamilika amwombe Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia aje auzindue huu mradi kwa sababu atakuwa ameweka historia kubwa, lakini ameweka heshima kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nimshukuru Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Engineer wetu, lakini nimshukuru sana Mkurugenzi wa RUWASA. Kwa kweli, huyu Mkurugenzi ni msikivu sana, anatusaidia sana na Mheshimiwa Waziri kwa kweli, ana Mkurugenzi ambaye anamfanyia kazi nzuri sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nina mambo mawili ambayo ningependa kuchangia leo. La kwanza, nimeshaeleza kuhusu hii miradi yangu ya maji, tuna huu Mradi wa Kintinku - Lusilile; huu mradi ulikaa miaka 15 ulikuwa umeshindikana kukamilika, mradi wa vijiji 11, lakini nimesema tumepewa bilioni mbili na mkandarasi yupo site ameshaanza kufanya ile kazi ya kumalizia. Amesaini mkataba wa kumaliza huu mradi ifikapo Oktoba mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nikuombe sasa tuisimamie Serikali, lakini nimwombe Waziri amsimamie mkandarasi. Nimshukuru yule mkandarasi aliyenipa ni msikivu sana, anafanya kazi nzuri sana. Kazi ilikuwa ngumu, lakini ameweza kuusukuma ule mradi.

Mheshimiwa Spika, tuna Mradi pia wa Miji 28 ambao na wenyewe tulipata pale Mamlaka ya Mji Mdogo wa Manyoni. Wakandarasi walishakuja, lakini nimwombe Mheshimiwa Waziri awasukume wale wakandarasi kwa kuwa wananchi wamesubiri sana huu mradi kwa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna vijiji ambavyo tumechimba visima vya maji kwa muda mrefu tumekosa. Kuna Kijiji cha Mpapa, Kijiji cha Igwamadete, Kijiji cha Mazwichii, Kijiji cha Kitalalo, Kijiji cha Magasai, kwa kweli, hivi vijiji tumefanya survey ya maji muda mrefu na kwa bahati mbaya hatujapata maji. Nimwombe Waziri sasa watafute namna ya kuhakikisha kwamba, hawa wananchi ambao wamesubiri muda mrefu kupata maji, tuje na ubunifu wa kuweza kuwasaidia waweze kupata maji.

Mheshimiwa Spika, suala la pili na la mwisho ni kuhusu Mfuko wetu wa Maji wa Taifa (National Water Fund). Wabunge wengi wanaposimama hapa kuchangia wanatamani kuona tunakwenda kutatua tatizo la maji kwenye Majimbo yao, ili tuweze kutatua tatizo la maji kwenye Majimbo yao tunahitaji kuwa na financing system ambayo iko very stable and sustainable. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunahitaji kumsaidia Mheshimiwa Waziri. Sheria ya kuanzisha Mfuko wa Maji ya 2019 inasema kwamba tutapata kutoka kwenye fuel levy angalau shilingi 50 kwa kila lita. Mimi naona tuna tatizo. Mfuko wa Maji wa Taifa ndiyo Mfuko ambao unatakiwa uwe very sustainable kwa ajili ya kusimamia miradi ya maji Tanzania. Ukiacha kwamba tunapata fedha kutoka kwa wafadhili, lakini hiki ni chanzo ambacho sisi kama Watanzania tunahitaji kukisimamia. Nadhani kuna jambo la kufanya kwenye huu Mfuko wa Maji.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni nini; kwanza tuna Jumuiya za Watumia Maji. Kwa mfano, kwa Manyoni nina Jumuiya moja ya Watumia Maji inaitwa Mkombozi, sasa hivi wana milioni 140 kwenye akaunti yao. Nina Jumuiya moja ya Watumia Maji kutoka Kijiji cha London, wana milioni 125 kwenye akaunti yao, nina jumuiya moja kutoka Sorya wana milioni 60 kwenye akaunti yao. Idea yangu ni nini kama tunataka kusaidia Mfuko wa Maji ku-expand ile financing mechanism yao tunahitaji vilevile ku-diversify, kutafuta vyanzo mbalimbali vya maji. Nashauri nini, zile fedha ambazo tunazikusanya kwa kupitia Jumuiya za Watumia Maji zinakuwa idle, kwa nini tusitengeneze mfumo zile jumuiya za maji vilevile zichangie kwenye Mfuko wa Taifa wa Maji? Ninashauri kwa kupitia hili tunaweza tukakusanya fedha nyingi ambazo hizohizo zitasaidia kwa ajili ya kuchimba visima kulekule na kwa ajili ya expand hata utoaji wa huduma ya maji vilevile. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukiangalia kwenye Sheria ya Kuanzisha Mfuko wa Maji, imetoa provision kwamba zaidi ya asilimia 88 ya fedha itakayokusanywa iende kwenye miradi ya maji, of which mimi naona ni kitu kizuri, kwamba tunaweza tukafanya mambo makubwa sana kwenye suala la kupeleka miradi ya maji. Kwa kupitia hili nina uhakika sasa kilio hiki cha Wabunge wengi kwamba miradi haikamiliki na kadhalika, nadhani tunaweza tukatatua. Mbali ya kutegemea fedha za wahisani tu, lakini tutakuwa na uhakika wa kutegemea fedha ambazo zinatokana na miradi yetu ileile ya kule. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho, mimi nirudie tena kumshukuru Waziri. Kwa kweli kwa sisi watu wa Kintinku – Lusilile kwenye ule mradi wako mkubwa wa bilioni 12 umetutendea haki sana. Ninakuombea wewe na Naibu Waziri wako muendelee kutusaidia, ule mradi wa maji ikifika Oktoba mwaka huu tukaweke historia na Mheshimiwa Rais aje auzindue ule mradi.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2022 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii ya kuwa mchangiaji wa mwisho kwenye Wizara hii ya Fedha. Kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais, Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika Taifa letu. vile vile, nimshukuru Dkt. Mwigulu, Waziri wetu wa Fedha pamoja na Naibu Waziri na timu yako yote kwa kazi kubwa ambayo wanaendelea kuifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nitachangia katika maeneo makubwa mawili. Eneo la kwanza nitachangia kuhusu mifumo ya ukusanyaji mapato hususani katika Serikali za Mitaa, lakini muda ukiniruhusu nitachangia kuhusu miradi mikubwa ya maendeleo na jinsi ya utoaji wa fedha kwenye hii miradi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunatambua kwamba Serikali imefanya mageuzi makubwa sana katika ukusanyaji wa mapato hususani katika Serikali za mitaa. Huko nyuma tulikuwa na mfumo ambao ulikuwa unaitwa Local Government Revenue Collection Information System ambao ulikuwa unatumika kwa ajili ya kukusanya mapato. Hivi karibuni watu wa TAMISEMI wameboresha ule mfumo wamekuja na mfumo unaitwa TAUSI. Nataka nianze kujikita kwenye ule mfumo wa mwanzo ambao tunakwenda kuu–phase out iwe lesson kwa ajili ya jinsi gani tunakwenda ku–take off na ule mfumo wa TAUSI ambao tunakwenda kuanza nao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri anajua kwamba katika mfumo wetu huu wa Local Government Revenue Collection Information System ulikuwa na changamoto nyingi sana. Changamoto ya kwanza ilikuwa ni suala la kutoa zile control number na hili nitatolea mfano kwenye ukusanyaji wa mapato. Naomba nitumie case study ya Manyoni. Katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki tuna wakusanya mapato ambao wameajiriwa na halmashauri. Wale wakusanya mapato wanapokusanya ili waweze ku–bank wanapewa control number. Kuna changamoto kubwa sana kwenye huu mfumo wa kukusanya mapato hususani kwenye control number.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ikoje? Kuna wakati kijana amekusanya milioni tano anakwenda na milioni tano mkononi, anapewa control number yenye thamani ya milioni moja. Tukiwauliza watu wa ICT wanakwambia mfumo upo down hauwezi ku-take up taarifa zote. Hili ni tatizo kubwa sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna baadhi ya Waheshimiwa Wabunge hapa wamechangia kwamba mwezi mzima mfumo uko chini malipo mbalimbali hayafanyiki. Kwa kweli tunatambua umuhimu wa mfumo huu wa ukusanyaji wa mapato, lakini na mfumo ambao unatumika kwenye malipo. Hata hivyo, nimshauri Daktari, nadhani sasa anahitaji kuja na mkakati rasmi wa kuhakikisha kwamba tunawezaje kuboresha huu mfumo wetu kwenye malipo na kukusanya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kuhusu huu mfumo wetu, mfumo huu ni mzuri sana, lakini nadhani kuna sehemu ambazo mess up. Inakuwaje wiki mbili mfumo uko down lakini hatuwezi kulipa? Kwa hiyo Mheshimiwa nimwombe Waziri akae na watu wake wa Wizara ya Fedha, watu wa IT kwa kushirikiana na BOT watuambie, tunawezaje kuufanya mfumo huu uwe user friendly na watu walipe kwa wakati?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa vijana wanapokusanya mapato hawatakiwi kukaa na fedha nyingi. Risk ikoje? Kijana amekusanya milioni tano anapokwenda kuomba control number aka–bank zile fedha anatolewa control number ya milioni moja, milioni nne anarudi nayo. What happened kwa Manyoni? Ilifika kipindi sisi tulikuwa na defaulters zaidi ya milioni 100 kwa mwaka. Watu ambao ukiwauliza hii hela mbona unadaiwa haamini kama anadaiwa. Kumbe kipindi kile alitolewa control number yenye value ya chini akajua labda hawa watu wamesahau ile milioni nne akaa nayo, muda ukaenda akaamua kuitumia. Hili ni tatizo kubwa. Kwa hiyo, namshauri Mheshimiwa Waziri, kwenye huu mfumo wa kukusanya mapato ambao wmeuanzisha sasa hivi wa TAUSI namshauri waende wakafanye maboresho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwapongeze TAMISEMI na Waziri wa Fedha, wameboresha huu mfumo wa zamani wa kukusanya mapato wamekuja na huu mfumo mpya ambao unaitwa TAUSI ambao halmashauri nyingi zimeanza kuutumia, lakini bado kuna changamoto moja. Mfumo huu unahitaji elimu itolewe kwa wananchi. Kwa mfano sasa hivi, business license zote zinatolewa kwenye mfimp wa TAUSI kila kitu, mfanyabiashara, fundi anatakiwa ajisajili kwenye mfumo wa TAUSI, ni wangapi wanaujua huu mfumo? Tunahitaji kutoa elimu kwa wananchi ili waujue huu mfumo na iwe rahisi ku–take off tunapoanza ile Julai kwa zile halmashauri ambazo bado hazijaanza kuzitumia ili ziweze kuutumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine kwenye huu mfumo wa kutoa control number, kama kijana anaweza akakusanya milioni tano anapokwenda anakuta system iko down au inatoa bili ambayo iko chini, ningeshauri watengeneze back up system kuliko hawa vijana kukaa na hela muda mrefu, inakuwa ni very risk kwao. Matokeo yake tunawaingiza kwenye risk ya kudaiwa na tunakuwa na defaulters wengi. Kwa hiyo nashauri waandae back up system ambapo kama mfumo uko down hawa vijana wasikae na fedha nyingi nyumbani tuwe na mfumo ambao tunaweza kwenda ku–bank, then wakafanya reconciliation. Lengo ni kuhakikisha kwamba tunapunguza misuse za fedha, lakini pia tunapunguza upotevu wa hizi fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo nataka kuchangia ni kuhusu miradi mikubwa ya maendeleo. Niishukuru sana Serikali, kwa Manyoni tumepata fedha nyingi sana. Tumepewa bilioni nne za Ujenzi wa Shule ya Wasichana ya Mkoa. Vile vile, tumepewa zaidi ya bilioni moja kwa ajili ya Ujenzi wa Chuo cha VETA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu anatambua Daraja la Sanza. Kwenye kila Ilani ya Uchaguzi huwa Daraja la Sanza linawekwa. Nafahamu sasa hivi lipo kwenye mchakato wa manunuzi. Nimwombe Waziri mwaka unapoanza sasa, huyo mkandarasi akapatikane na ujenzi wa daraja la Sanza uweze kuanza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili na Mheshimiwa Waziri anatambua kuna Mradi pale Mwahalala, Kituo cha Pamoja cha Ukaguzi wa Magari. Ule Mradi wa zaidi ya bilioni 30 ulisimama tangu mwaka 2016. Pale kuna majengo yanaendelea kuoza. Sasa ningeshauri kwenye bajeti hii ingawa sijaona anapoelezea, naomba Waziri anapokuja ku–wind up atuambie, nini mpango wa Serikali kuuendeleza ule mradi ambao umesimama tangu mwaka 2016.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale kuna nyumba, tunashauri kama Serikali imeacha huu mradi waturuhusu zile nyumba zitumiwe na watumishi. Tuna Shule za Sekondari, Shule za Msingi, zahanati, nyumba zile zinaweza zikatumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, kuna huu Mradi wa Mji wa bilioni 12 wa Kintinku-Lusilile. Kwanza, namshukuru sana Waziri wa Fedha, kwa kweli kwenye huu mradi ametusaidia sana na sasa hivi mkandarasi yuko site ameanza kazi. Hata hivyo, bado mkandarasi anadai zaidi ya bilioni tano ili aweze kukamilisha huu Mradi. Kwa hiyo nimwombe Mheshimiwa Waziri, kwenye huu mradi ambao unakwenda kwenye vijiji 11 ambao una zaidi ya miaka 15 haujakamilika, atusaidie ili uweze kukamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niendelee kumpongeze sana Mheshimiwa Rais, lakini nimpongeze Mheshimiwa Mwigulu na timu yake na naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kipekee nikushukuru sana kwa kunipa hii nafasi, lakini nichukue nafasi hii nimshukuru sana ndugu yangu Mheshimiwa Nape, Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa ambayo wanaifanya. Vilevile niwashukuru sana ndugu zetu wa USCAF, TTCL na timu nzima ya Mheshimiwa Nape ambayo kwa kweli wanafanya kazi kubwa. Hatuna mashaka na Mheshimiwa Nape, tunajua alivyo aggressive, alivyo determined na amedhamiria kubadilisha hii Wizara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nina mambo machache. La kwanza, naomba nijadili kuhusu umuhimu wa hii Wizara. Sasa hivi ukiangalia Tanzania tulipo, Wizara hii ya TEHAMA ndio engine ya maisha yetu ya kila siku, ni engine ya uchumi, ni engine ya mawasiliano, ni engine ya kila kitu. Sasa wakati nafikiria ni jinsi gani nakuja kuchangia kwenye hii Wizara, nilikuwa naangalia hii Wizara nai-position wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia Wizara zote, zinategemea Wizara ya Mheshimiwa Nape. Watu wa fedha wanamtegemea Mheshimiwa Nape, watu wa afya wanamtegemea Mheshimiwa Nape, watu wa kilimo wanamtegemea Mheshimiwa Nape, watu wa maji wanamtegemea Mheshimiwa Nape. Hii ni Wizara ambayo ni pivotal. Ni Wizara ambayo ipo at the center. Mheshimiwa Nape ni refa anayehakikisha kwamba ili utoaji wetu wa huduma unaotolewa kwa njia ya TEHAMA, Wizara ya Maji, Wizara ya Kilimo, Wizara ya Afya, unafanikiwa lazima tumwezeshe Mheshimiwa Nape. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kubwa ni nini? Sisi kama nchi tunahitaji kui-brand hii Wizara. Hii ndio Wizara mama, Wizara ambayo imebeba maisha yetu, Wizara ambayo imebeba uchumi wetu. Hapa tunaongea kwa kutumia hii technology ni kwa sababu imewezeshwa na Wizara ya Mheshimiwa Nape. Tunatumia vishikwambi ni kwa sababu ya Wizara ya Mheshimiwa Nape. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wito wangu ni nini kwa Serikali? Kwanza nina mambo mawili; la kwanza, ufike muda sasa tufanye reformation ya hii Wizara. Hii Wizara inatakiwa kukaa kwenye muundo upi? Hii Wizara inatakiwa ikae katikati i-coordinate zile Wizara zote, lakini sidhani kama hiyo structure, hiyo business modal na coordination modal imekuwa well defined. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naishauri Serikali ifikirie upya tunai-position vipi Wizara ya TEHAMA ili kuhakikisha kwamba sasa inajionesha na inatoa ile coordination support vizuri sana katika Wizara nyingine? Hilo lilikuwa la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili, kwanza nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri. Mwaka 2021 alinitengea fedha kwa ajili ya kujenga minara ya simu kule Mangoli na Heka kwa kupitia TTCL na tayari tumeshajenga ile minara. Mnara wa Mangoli umeshaanza kufanya kazi, mnara wa Hika umeshakamilika na tunasubiri kuuwasha. Bado kuna maeneo yana shida sana ya mitandao. Kuna Kijiji cha Igwamadete, Simbangulu, Mbweko, Magasai, Kapiti na vingine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii nimshukuru vilevile Mheshimiwa Waziri, katika bajeti hii hivi vijiji vyote ameviingiza kwenye bajeti, nashukuru sana. Wito wangu ni nini? Wengi wameongea hapa, sidhani kama tunahitaji kujenga kila aina ya mnara, Vodacom, TTCL kwenye kila Kijiji. Tunahitaji ku-integrate hizi services. Kwa hiyo, wito wangu kwa Mheshimiwa Nape, kaa na timu yako m-brainstorm, mje na modal ambayo itakuwa very cost effective kuhakikisha kwamba, Voda, Halotel, TTCL, watatumia mnara mmoja, hiyo itatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. (Makofi)
Makadirio na Mapato ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaishukuru Serikali imeandaa sera na sheria kwenye sekta za TEHAMA, sayansi na ubunifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili Serikali iweze kuisimamia vizuri sekta ya TEHAMA tunahitaji kwa haraka sana kuanzisha ICT Professional Regulation (ICT Commission haijafanya kazi ya kufanya regulations) imara kama wenzetu kwenye sekta zingine mfano wahasibu, afya, na kadhalika. Tumeona CAG akiibua mambo kibao kuhusu mifumo yetu ya taarifa/TEHAMA tunaweza kuhakikisha maadili na weledi kwenye sekta ya TEHAMA bila kuwa na Bodi ya kuwasimamia waatalamu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna mwingiliano mkubwa wa majukumu kati ya baadhi ya taasisi za Serikali mfano TCRA, eGA, COSTECH, ICT Commission na Wizara za Utumishi, Elimu na Mawasiliano. Ni vizuri tukawa na taasisi moja inayosimamia au kupunguza mwingiliano na kutumia vizuri rasilimali

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunashukuru Serikali kuanzisha matukio mbalimbali ya kuinua vipaji (innovation weeks) kwa mfano MAKISATU ambapo vijana wameonesha matumizi ya TEHAMA na ubunifu mwingine kusaidia sekta za elimu, afya na kadhalika. Changamoto kubwa ni kuweza kuwa na mfumo mzuri wa kitaasisi na endelevu wa kuwatambua na kuwaendeleza wale wenye products/innovations ambazo zitakuwa na faida kwa vijana hawa na Taifa kwa ujumla. Iko wapi Silicon Valley ya Tanzania? Ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2021 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, nami nachukua fursa hii kushukuru sana kwa kunipa hii nafasi ya kuchangia, kipekee sana nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa ambayo anaifanya, katika Jimbo letu la Manyoni Mashariki ameweka impact kubwa sana. Nichukue nafasi hii nimshukuru sana Dkt. Mwigulu Nchemba na Naibu Waziri wako kwa kazi kubwa kwa kuja na bajeti ambayo ina ubunifu mkubwa sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo nina mambo takribani matatu ya kuchangia, eneo la kwanza nitachangia kuhusu tathmini ya vyanzo vya mapato ambavyo tulipitisha mwaka uliopita, nitachangia kuhusu namba ya mlipa kodi (tax identification number), nitachangia vilevile kuhusu ile asilimia 10 ya mapato ya Halmashauri inatokana na asilimia 40 ya maendeleo na mwisho nitachangia kuhusu suala la mishahara binafsi.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba mwaka jana tulipitisha vyanzo vya mapato, mojawapo ya vyanzo vya mapato tulipitisha tozo kwenye miamala ya simu na wewe ulikuwa kinara uliita tozo ya uzalendo. Pia tulipitisha mfumo wa kubadilisha ukusanyaji wa kodi za property tax, kutoka TRA lakini tukapeleka kwenye mfumo wa LUKU. Sasa sikusikia kwenye taarifa yako Daktari kwamba kwa kiwango gani tumeweza kufanikiwa na hivi vyanzo ambavyo tulivi-propose ili sisi itusaidie kuja na mfumo ambao tunaweza tukaboresha zaidi whether tunahitaji kuendelea na miamala ya simu na efficacy yake ilikuwaje, vilevile kodi ya majengo ni jinsi gani imekuwa effective, niliona hilo nimshauri Waziri anapokuja ku-wind up tujue kwamba to what extent hizo tozo na hizo kodi zimekuwa effective na unashauri nini tuendelee nazo au zibaki.

Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili ni suala la Namba ya Mlipakodi. Kumekuwa na sintofahamu kubwa na kumetokea taharuki kwa wananchi, lakini mimi naomba niwatoe mashaka, nimepitia nchi mbalimbali ambazo zinatumia TIN Number katika mazingira tofauti. Kwa mfano, UK wana kitu kinaitwa National Insurance Number (NINO) ile NINO ndiyo inatumika kama substitute ya TIN Number. Nchi ya Hong Kong wenye hawana ID zingine wanaita Hong Kong Identity Card ileile Hong Kong Identity Card ndiyo inatumika kama TIN number, the same to Pakistan, the same kwa USA.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema nini hapa? Kwanza niseme idea aliyokuja nayo Daktari Mwigulu Nchemba is the valid idea na tumechelewa sana. Tumechelewa kwa sababu gani, nilitegemea kwanza tuondoe utitiri wa vitambulisho tulivyonavyo, mimi nina vitambulisho zaidi ya vitano vyenye Namba nina cheti cha kuzaliwa, nina employers ID number, nina Social Security Number, nina Leseni ya Udereva na zingine huu ni utitiri mkubwa sana. Nchi zingine wanachofanya mtoto anapozaliwa anapewa TIN number ile TIN number inakuwa the same kote huko, ukimwajiri atatumia the same TIN number, kwenye social security atatumia the same TIN number. Lakini kumekuwa na upotoshaji mkubwa kwenye mitandao, watu wanajua hii idea ya TIN number ni kwamba watu wanakuja kulipa head tax, kodi ya kichwa siyo kweli. Kwa hiyo, mimi niwaombe Waheshimiwa Wabunge kwamba tu-harmonize hii mifumo tusiwe na vitambulisho vingi, kama inawezekana cheti cha kuzaliwa, mtoto anapozaliwa apewe TIN number atakutana nayo akishakua mtu mzima huko atalipia kwenye mapato. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nilipenda kuchangia suala la asilimia 10. Nimewasikia Wabunge wenzangu wakichangia asilimia 10, mimi namuunga mkono Daktari Mwigulu Nchemba. Kwanza ninaishukuru Serikali kutenga ile asilimia 40 ya maendeleo kwenye mapato ya ndani, ambapo asilimia 10 tunaenda kukopesha katika ile 4-4-2. Tukumbuke kwamba hizi fedha tunaenda kuzikopesha lakini hawa watu tunapowakopesha hizi fedha hawana miundombinu ya kufanyia kazi, hakuna masoko, hakuna vibanda vya Mama Ntilie kufanya biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Dkt. Mwigulu amekuja na idea kwamba badala ya kuchukua yote asilimia 10 uipeleke kwenye mikopo, ambayo nitailezea baadae, ame-propose asilimia Tano ya ile hela iende ikaweke miundombinu kwa ajili ya hawa ambao tunaenda kuwakopesha. Unakikopesha kikundi hakina soko, unawakopesha mama ntilie hawana sehemu ya kupika matokeo yake anaenda kutumia gharama nyingi kulipia pango la kile kibanda cha kufanyia biashara. Kwa hiyo, mimi naunga mkono wazo kwamba tuchukue asilimia tano ya mapato yale ya asilimia 10, tukaweka zile infrastructure, lakini kuna multiply effect kubwa kwenye hili, watu wengi watanufaika na lile soko kuliko vikundi. Nitakutolea mfano, katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki….

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Matiko Taarifa.

T A A R I F A

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe taarifa mchangiaji kwamba dhana kuu ya asilimia 10 ilikuwa ni kuwainua wananchi kiuchumi, lakini hizi asilimia tano anazosema kwamba zinakwenda kwenye miundombinu ya masoko kwamba watu waende kuuza pale, wengine wanakopa wanafuga nguruwe, wengine wanafuga kuku, products ambazo haziendi kwenye hayo majengo ambayo anaelekeza. Kwa hiyo, nimependa kumpa tu hiyo taarifa kwamba sio wote wanaokopeshwa wanakwenda kwenye umachinga. (Makofi)

SPIKA: Dkt. Chaya.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, partially naunga mkono hoja ya dada yangu, lakini naomba nimweleze kitu kimoja wale watu wanakopeshwa kwa kutumia revolving system, zile fedha zinarudishwa. Nitatolea mfano, kule Manyoni, tumeshakusanya fedha kutoka kwa wale ambao waliokopa, zile fedha zikirudi wanakwenda kukopeshwa wale tena. Hoja yangu ni nini, hatuna miundombinu ya hawa watu katika kufanya biashara. Kwa hiyo, bado naunga mkono kwamba tutenge asilimia tano kwa ajili ya kuwasaidia kujenga masoko, kujenga vibanda ile fedha ambayo inarudishwa itatumika kwa ajili ya kukopesha na tutaongeza capacity ya kukopesha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine ambalo ni la mwisho ni kuhusu hii mishahara binafsi, wenzangu wamechangia kuhusu mishahara binafsi na naunga mkono hoja. Kuna matatizo mawili katika mishahara binafsi hususani kwa wale ambao walitolewa kwenye utumishi wa umma, hususani wale ambao walishushwa vyeo vyao. Kwanza kuna hoja kubwa tatu hoja ya kwanza, huyu mtu wakati anateuliwa je, alikuwa ameajiriwa? Hoja ya pili ni kwamba, je, kama alikuwa ameajiriwa? Tatu, je, alikuwa ameajiriwa wapi ni Serikalini au kwenye private sector? Nne, wakati tunamteua nini tofauti ya mshahara wakati anateuliwa na kule alikokwenda? Hizo ndio hoja kubwa nne ambazo tunahitaji kuangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lingine watu wakishateuliwa anakuwa na mshahara mkubwa, anaamua kwenda kukopa, kwa hiyo, kuna burden ya mikopo ambayo mtu huyu anakuwa nayo. Tatizo ni kwamba na nakubaliana nalo kwamba tumekuwa na watu wengi ambao wapo mtaani, wametolewa kwenye mfumo wanapokea mishahara mikubwa ambayo ni burden kwa nchi. Kwa mfano, katika halmashauri moja wakati fulani kulikuwa kuna Wakurugenzi wanne wote wanapokea mshahara sawa, hiyo ni burden kubwa kwa nchi. Ushauri wangu ya kwanza, tuandae mwongozo mpya ambao sasa utakuja kusaidia idea ambayo Mheshimiwa Dkt. Mwigulu anayo kwamba kama mtu ametenguliwa, je… (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Ahsante Dkt. Chaya kwa mchango mzuri.

MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025 na Mapendekezo ya Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2024/2025
MHE. DKT. PIUS S. CHAYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi natumia nafasi hii kukushukuru wewe, lakini kipekee nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kazi kubwa ambayo anaifanya katika Taifa letu la Tanzania lakini katika Jimbo langu la Manyoni Mashariki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niwashukuru hawa ndugu zangu wawili, Profesa Kitila na Daktari Mwigulu kwa kazi kubwa ambayo mnaifanya ya kumsaidia Rais katika hizo Wizara mbili nyeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi leo nina mambo machache sana na nitaanza na Profesa Kitila. Kwa Profesa Kitila nimekuwa nikitafakari ni jinsi gani tunaandaa hii miradi yetu mbalimbali kila mwaka kupitia, mpango wa maendeleo wa kila mwaka ambao tumeuvunja kwenye ule mpango wa maendeleo wa miaka mitano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la kwanza huwa natafakari unakuta kwenye kijiji kimoja tumepeleka miradi mitatu, Mradi wa Maji, Mradi wa Umeme, Mradi wa Barabara lakini ukiangalia hii miradi yote haisomani, kwa lugha nyingine hakuna convergency.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ningemshauri Mheshimiwa Waziri Profesa Kitila, katika eneo ambalo Wizara ya Mipango inahitaji kutusaidia ni kuhakikisha kwamba kunakuwa na convergency invent. Kwamba tunapoenda kwenye kijiji kimoja Mheshimiwa Rais amepeleka Mradi wa Maji, Mradi wa Umeme, Mradi wa Afya nini interpretation ya wananchi wa pale in terms of invent, hilo ni eneo la kwanza ningeliomba Mheshimiwa Waziri ulifanyie kazi. Tunahitaji kuja na framework ambayo ita-tap hizo convergency intervention zote tuone ni jinsi gani wananchi wapo satisfied na ile miradi yote iliyoenda katika eneo moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni suala la agenda ya vijana (youth agenda). Tumeshafanya mambo mengi sana, Mheshimiwa Rais amefanya mambo makubwa kwenye huduma za jamii, ninategemea sasa na ni matarajio yangu na ni matumaini yangu kuona huu mpango sasa una-move kutoka kwenye huduma za jamii kwenda kwenye agenda ya kuwaendeleza vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, agenda ya vijana ni global agenda na hasa hasa kwenye masuala ya kuwajenga kiuchumi. Kuna maeneo mawili nchi za wenzetu wamefanya na hasa hasa vijana ambao wapo out of the school. Tuna kundi kubwa la vijana waliomaliza shule ya msingi hawakufanikiwa kuendelea sekondari, waliomaliza sekondari hawakufanikiwa kuendelea vyuoni wapo mtaani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri mambo mawili, la kwanza tunahitaji sasa kuja na comprehensive program kwenye masuala ya elimu ujuzi. Katika hili eneo Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya, lakini bado kuna changamoto. Changamoto ya kwanza tunawachukua vijana kutoka vijijini wanaenda kusoma Singida Mjini, kuna wengine wanashindwa kule kwa sababu ya gharama. Kwa nini tusianzishe program kama hizo za kuwajngenea ujuzi katika maeneo yao, kwenye zile locality zao, kwenye kata, kwenye tarafa ili kuwapunguzia huo mzigo wa wenyewe kusafiri kwenda kule.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, eneo ambalo tunaweza tukalifanya vizuri sana na tukaja na mradi mkubwa wa kuwasaidia vijana wa kitanzania hasa wale waliomaliza shule ya msingi, waliomaliza sekondari hawakufanikiwa kwenda kwenye vyuo vya juu, ni kuwajengea ujuzi kwa kupitia mafunzo ya muda mfupi, miezi miwili, miezi mitatu, wakitoka pale tunaweza tukawa-link kwenye viwanda mbalimbali ambavyo vipo hapa. Hili ni eneo ambalo ni muhimu sana linaweza likatusaidia sana kwenda na hii agenda ya vijana ili tuweze kuwasaidia vijana wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ni eneo la mradi wa BBT wa Bashe. Mheshimiwa Bashe idea yako ya BBT it is a very brilliant idea, lakini Mheshimiwa Bashe usipokuwa makini na hii idea you will fail. Naomba nikushauri kitu kimoja, hii idea ni brilliant sana kwa sababu kwanza una-address youth agenda lakini kuna tatizo moja la selection bias. Umewahamisha vijana kutoka Manyoni umewapeleka Morogoro that is not sustainable. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeshauri tu-focus kwenye maeneo yao tujikite kwenye ile local economic development. Kama aneo ni potential kwa kilimo wakusanye wale vijana wanaotoka kwenye lile eneo BBT ifanye kazi kwenye lile eneo, lakini kuwatoa Manyoni kuwaleta Dodoma, kuwatoa Manyoni unawapeleka Morogoro kimsingi haitakuwa endelevu. Kwa hiyo, hili ni eneo ambalo mimi ningekushauri kwamba Serikali iweze kulifanyia kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho ushauri kwa ndugu yangu Daktari Mwigulu kwenye suala la bajeti, tuna miradi mingi ambayo umeitaja pale Serikali inaenda kuitekeleza lakini kwa upande wa Manyoni mimi ningeshauri jambo moja. Tuna miradi ambayo imetajwa sana kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa mfano Daraja la Sanza, kila mwaka Daraja la Sanza kila awamu Daraja la Sanza huwa linatajwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimshukuru Mheshimiwa Rais safari hiii, ameruhusu angalau mkandarasi ameshapatikana sasa tunaomba Daraja la Sanza liende likaanze kujengwa. Kuna Daraja la Ngonjigo chini ya TARURA vilevile kuna Bwawa la Mbwasa Mheshimiwa Bashe, hili bwawa kwenye kila Ilani ya CCM lipo. Nakushukuru na wewe mwaka huu naona umeshaliweka sasa nategemea kwamba kwenye bajeti hii sasa litaenda kutekelezwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho Mheshimiwa Dkt. Mwigulu kuna huu Mradi wako wa Mwalala, kituo cha pamoja cha ukaguzi wa magari. Huu mradi ni wa zaidi ya bilioni 30 ulisimama tangu 2016 ulishafikia asilimia 60 mmetumia zaidi ya bilioni tano imeshakuwa pori pale. Nikuombe Mheshimiwa Dkt. Mwigulu zile ni fedha za watanzania twende tukauokoe huu mradi wananchi wanalalamika kwa nini mradi ulisimama tangu 2016 na mradi una tija naomba sana huu mradi safari hii kwenye bajeti hii, twende tukau-revival uanze kufanya kazi kwa sababu ni mojawapo ya miradi ambayo ina tija sana kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nirudie kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini niwashukuru hawa Mawaziri wawili Profesa Kitila na Daktari Mwigullu kwa kazi kubwa mnayoifanya. Baada ya kusema haya naunga mkono hoja ahsante sana. (Makofi)