Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Contributions by Hon. Godwin Emmanuel Kunambi (29 total)

Hotuba ya Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli aliyoitoa wakati wa Ufunguzi wa Bunge la Kumi na Mbili, Tarehe 13 Novemba, 2020
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa nimshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema, aliyenijalia afya njema hata siku ya leo nikawa hapa. Pia naomba niunge mkono hoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma hotuba zote mbili za Mheshimiwa Rais. Mheshimiwa Rais kupitia Serikali yake ya Awamu ya Tano anapojenga SGR maana yake anafanya capital investment, anapojenga Bwawa la Kufua Umeme la Nyerere anafanya capital investment; anapojenga na kuimarisha bandari zote anafanya capital investment; anavyonunua ndege anafanya capital investment. Hii tafsiri yake ni nini? Nchi hii miaka ijayo hatuna tena changamoto kwenye suala zima la ukuaji wa uchumi wa nchi yetu kwa sababu Mheshimiwa Rais ameshatuwekea misingi bora ya kukua kwa uchumi wetu na Taifa letu. Kwa hiyo itoshe kusema katika hili nampongeza sana Mheshimiwa Rais na namwombea Mungu amjalie Maisha mema.

Mheshimiwa Naibu Spika, kimsingi Serikali ya Awamu ya Tano imefanya mambo makubwa sana kwenye sekta mbalimbali. Ushauri wangu ni eneo moja ambalo linahusu mgawanyo wa huduma hizi kitaifa. Tukifanya tathmini ya ujenzi wa barabara, huduma ya afya, elimu, kitaifa utaona kwamba kuna baadhi ya watu lugha hii hawaielewi. Nikisema tumejenga vituo vya afya kadhaa kitaifa, mwananchi wa Jimbo la Mlimba ambaye hana kituo cha afya haelewi lugha hii. Ukisema tumejenga lami kiwango cha urefu kadhaa, maana yake mwananchi wa Mlimba ambaye tangu azaliwe hajaona lami hawezi kuelewa lugha hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa rai yangu na ushauri wangu na kwa sababu jukumu langu kama Mbunge ni kuishauri Serikali na kwa kuwa tunakwenda kufanya maandalizi ya Mpango wa Taifa, nashauri Wizara husika, hasa Wizara ya Fedha na Wizara nyingine za kisekta, umefika wakati sasa tutazame mgawanyo na uwiano wa huduma hizi kitaifa ili lugha hii kila mwananchi Mtanzania aielewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, nasema hivi kwa sababu kama walipa kodi ni Watanzania wote. Sasa inaleta changamoto kidogo mwananchi wa Mlimba anayelipa kodi ikaenda kujenga Dar es Salaam na yeye kimsingi ni mwananchi ambaye ana haki ya kupata huduma zote mbalimbali. Kwa hiyo nishauri tunapokwenda kuandaa na ni rai yangu na naamini kupitia Mawaziri hawa mahiri kabisa, hii hoja wataichukua, kwamba tunakwenda kupanga mpango wa kitaifa sasa, tutazame mgawanyo wa huduma hizi kitaifa ili Watanzania wote wanufaike na rasilimali za nchi hii, kwa sababu Serikali yetu siyo Serikali ya majimbo, Serikali ya majimbo ndiyo inahamasisha uneven development.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijikite katika eneo lingine la pato ghafi la Taifa. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri, Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Mambo ya Nje; hakika anafanya kazi kubwa sana. Ana spidi kali sana, lakini jamani wakati sisi wengine we are lagging behind. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unapozungumzia maendeleo ya Taifa letu lazima Wizara zote tuwe na muunganiko wa pamoja, tuzungumze lugha moja, ili tuhakikishe nchi yetu inakuwa kwa maendeleo kwa kasi zaidi. Kwa mfano, Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje anashughulika sana na kuimarisha mahusiano ya nchi yetu na nchi zingine, kupata wawekezaji wa kigeni. Hata hivyo, inapofika Wizara husika kuharakisha mchakato huo ili mwekezaji wa kigeni awekeze kuna masuala ya nenda rudi, njoo kesho, unajua muda pia ni mali; muda ni mali. Leo siyo kesho, siku ya leo haitapatikana tena kesho. Kwa hiyo ni rai yangu kwamba Wizara zingine zina kila sababu sasa ya kuona zinachangia kasi hii ya Wizara ya Mambo ya Nje, hasa kwenye suala zima la uwekezaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka kusema nini hapa; ukisoma hotuba ya Mheshimiwa Rais ukurasa wa tisa utaona ameeleza namna ya ukuaji wa pato la Taifa kutoka trilioni 94.3 kwa mwaka 2015 hadi trilioni 139.9 mwaka 2019. Tunampongeza Mheshimiwa Rais, lakini swali langu na hoja yangu ya msingi hapa, tunapopima ukuaji wa uchumi wa nchi turudi tujikite kuona hasa kwenye suala zima la export na import. Tuone ni kwa kiwango gani tunauza bidhaa zetu nje na kiwango gani tunaagiza bidhaa ndani ya nchi. Kwa mfano, import ikiwa kubwa kuliko export matokeo yake unakuwa na unfavorable balance of payment. Hoja yangu; tuongeze uzalishaji kwenye sekta za kilimo, kwenye sekta za mifugo, kwenye sekta mbalimbali ili tuweze kukuza pato letu la Taifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijikite kwenye Sekta ya Ardhi. Ardhi tuna fursa kubwa; nishauri tu, tuna kila sababu ya kupima nchi hii kwenye halmashauri zote na jambo lenyewe ni dogo sana. Watanzania wakipata hatimiliki Serikali itaongeza tax base na mwananchi wa kawaida anaweza kukopesheka benki na hii ikasaidia uchumi wa nchi yetu kukua.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninapokwenda kuhitimisha naomba niende moja kwa moja kwenye Sekta ya Barabara. Bado nisisitize Mkoa wa Morogoro ni mkoa wa kimkakati, ni mkoa ambao unalisha Taifa letu, hasa Jimbo la Mlimba. Barabara inayounganisha Mikoa ya Morogoro na Njombe kutoka Ifakara, kilometa 125, ni barabara ya muhimu sana kitaifa. Kwa hiyo rai yangu barabara hii ikijengwa itafungua uchumi wa nchi yetu, lakini pia wananchi wa Mlimba watanufaika na barabara hii. Kwa hiyo kwa kuwa barabara hii imeelezwa kwenye Ilani ya Chama Cha Mapinduzi Ibara ya 76, ombi langu, Wizara husika ya Ujenzi tunapokwenda kwenye Mpango sasa wa Taifa ni vyema kwenye bajeti yetu tukaanza ujenzi wa barabara hii ili Watanzania hawa wanufaike na barabara hiyo kitaifa.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalize kwenye Sekta ya Elimu. Jana mzee wangu, Mheshimiwa Dkt. Kimei ameeleza hapa, lakini changamoto kubwa hatuwezi kuboresha elimu, hasa kwenye Sekta ya Ufundi kwa kuanzia kwenye tertiary education. Wenzetu Wachina wana kitu kinaitwa industrial culture na kupitia All Chinese Youth Federation, ukisema uanzie kwenye tertiary education kuimarisha elimu ya ujuzi au ufundi mchundo, hatuwezi; tuanze na level ya shule ya msingi. Kuanzia shule ya msingi kuwe na study maalum tuwekeze kwa watoto wadogo, anapokua anakuwa na industrial culture, anavyokua inamsaidia yeye kukuza kipaji chake. Tunapoendelea kuwekeza kwenye sekta ya elimu ya juu, sisemi haina umuhimu, lakini maana yake tunatengeneza Taifa lenye mameneja wengi kuliko wazalishaji. Matokeo yake hawa mameneja hawana wa kuwasimamia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu kwamba tujikite, Wizara ya Elimu mama yangu yupo hapa, naomba atusaidie. Ikiwezekana vyuo vya VETA nayo iwe elimu bure, wasilipe chochote na ujenzi wa vyuo vya VETA, vijengwe kwenye ngazi ya tarafa, hasa Jimbo langu la Mlimba, Tarafa za Mngeta na Mlimba. Naeleza haya ili kuona namna gani tunaweza kuona Taifa letu linakwenda mbele.

Mheshimiwa Naibu Spika, nina hoja moja ya mifugo. Ni kweli tumekuwa nchi ya pili kwa ufugaji, lakini Mheshimiwa Rais ameeleza kwenye hotuba yake kwamba hataki kuona wafugaji, wakulima, wanahangaika. Leo hii unaona mfugaji anayefuga mifugo anaambiwa apunguze mifugo badala ya kumpa njia mbadala kwenye mifugo yake anayofuga.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye kilimo hali kadhalika; kilimo chetu bado kinahitaji kuongezeka thamani.
Kwa mfano pale Mlimba…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Kengele ya pili?

MBUNGE FULANI: Endelea.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kaka yangu, Mheshimiwa Bashe nisikilize hapa kidogo…

NAIBU SPIKA: Muda wako umeshaisha Mheshimiwa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Umeisha?

NAIBU SPIKA: Ndiyo. Ahsante sana.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naomba kuwasilisha. (Makofi)
Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2021/2022 – 2025/2026
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya njema hadi siku ya leo nikapata fursa ya kutoa mchango huu.

Mheshimiwa Spika, mimi nijielekeze moja kwa moja kwenye sekta ya kilimo. Unapozungumzia sekta ya kilimo kwenye taifa letu unazungumgumzia sekta muhimu sana, hasa ukizingatia zaidi ya Watanzania asilimia 65 wanashughulika na sekta ya kilimo.

Mheshimiwa Spika, unapozungumzia kilimo kuna mambo ya msingi hapa ya kuzingatia. Jambo la kwanza ni suala zima la utafiti, jambo la pili ni pembejeo na la tatu ni masoko; lakini wanavyokwenda kwenye masoko utagusa kidogo na masuala ya viwanda.

Mheshimiwa Spika, tunavyozungumzia tafiti mimi najiuliza maswali mengi sana hapa. Tumekuwa tuzijenga hoja za tafiti kwenye kilimo. Hatuna changamoto ya tafiti, tuna vyuo ambavyo vipo hapa kama vile Chuo Kikuu cha Sokoine (SUA) ni maelekezo tu. Wenzetu Japan kule wana mfumo mmoja ambao wanasema Public Private Academia. Maana yake nini, kuna umuhimu wa wasomi kufanya tafitil; tungetumia vyuo vikuu vyetu hivi kufanya tafiti, hamna haja ya fedha eneo hilo. Wape maelekezo SUA wafanye tafiti kwenye kilimo tuwekeze tupate kilimo chenye tija kwa taifa letu. (Makofi.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine nimezungumzia suala la pembejeo. Bado kuna changamoto kubwa ya pembejeo lakini kubwa zaidi ni masoko.

Mheshimiwa Spika, nirudi kwenye zao hili la kimkakati la mpunga. Ukizungumzia Mkoa wa Morogoro hasa Jimbo la Mlimba, sisi katika taifa hili tunalisha zao la mpunga. Hata hivyo tuna changamoto ya kuuza mpunga nje ya nchi, lakini hatuwezi kuuza mpunga mpaka tuuchakate mpunga. Kwa hiyo naiomba Wizara ya Kilimo itusaidie. Jimbo la Mlimba tungeweza kufanikiwa sana kama tungewekeza viwanda vya kuchakata mpunga tupate mchele, mchele uwekwe kwenye fungashio actually uwe branded na upelekwe nje ya nchi.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa najaribu kuona hapa wenzetu Japan wanaagiza chakula cha mwaka mzima, nilisema hapa awali, Zimbabwe wamekuwa wadau wakubwa wakiuza chakula nje ya nchi, na sisi tunaweza kufanya hilo; kwa hiyo tuongeze jitihada za utafiti kwenye kilimo, pembejeo lakini pia na viwanda pamoja na suala zima la masoko.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo ninataka niliguse ni eneo la viwanda. Eneo hili nitagusa wizara mbili, Wizara ya Ulinzi lakini pia na Wizara ya Viwanda na Biashara. Naomba kama kuna Waheshimiwa Mawaziri na Manaibu Mawaziri mnisikilize kidogo.

Mheshimiwa Spika, katika safari ya maisha yangu mnamo mwaka 2002 niliwahi pita pale Nyumbu. Nyumbu pale kuna Shirika la Nyumbu la Taifa. Shirika la Nyumbu la Taifa, yaani Nyumbu Automobile Engineering, mimi nimekaa pale miezi minne; nchi hii ni Tajiri. Kama Shirika la Nyumbu likatumika vizuri hatuwezi kuagiza magari Japan. Pale Shirika la Nyumbu linavifaa vyote lina foundry zote, linafanya hata iron processing. Kuna Electrical Furnace ambayo kazi yake ni kuchakata chuma. Wana-pattern shop, wana-foundry shop, wana kila kitu. Mheshimiwa Baba wa Taifa alianzisha shirika hili ili tuweze kupata magari ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kama tunafikiri kuna eneo la kuwekeza ili tupate fedha ni Shirika la Nyumbu. Kwa hiyo Waziri wa Ulinzi na Waziri wa Viwanda mtusaidie kufufua Shirika la Nyumbu ili Watanzania tusinunue magari nje ya nchi tununue ndani ya nchi yetu. Labda niseme tu, kwenye uchumi mtanisaidia. Suala la mauzo nje ya nchi na kuagiza bidhaa nje ya nchi; Mheshimiwa Waziri wa Fedha kaka yangu Mheshimiwa Mwigulu Nchemba naomba unisikilize eneo hili. Kwenye uchumi kuna masuala tunazungumzia kuna jambo la export na import nchi yeyote yenye uchumi imara lazima izalishe na kuuza sana nje ya nchi. Ukiona mnaagiza sana kuliko kuuza nje ya nchi maana yake nini, ukikokotoa pale, kuagiza bidhaa nje ya nchi idadi ya bidhaa zinazouzwa nje ya nchi ikiwa kubwa kuliko idadi ya bidhaa tunazonunua unapata favorable balance of payment, favorable balance of payment, maana yake unapata jibu chanya na siyo hasi, eneo hili wachumi watanielewa kidogo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tukiendelea kuagiza sana kuliko kuuza bidhaa nje ya nchi bado tutaendelea na uchumi ambao unatusababishia kuwa unfavourable balance of payment na mwisho wa siku nchi yetu itapata tatizo la capital flight. Capital flight kwenye uchumi maana yake unavyoagiza bidhaa nje ya nchi unachukua pesa ya ndani ya nchi kwenda kubadilisha na pesa...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: …ya nje ya nchi yaani dola maana yake nini ndani ya nchi hiyo utapata changamoto ya balance of payment.

Mheshimiwa Naibu Spika; naomba nimalizie kwa jambo moja, dada yangu hapa Mheshimiwa Halima Mdee amezungumza jambo ambalo Mungu anisaidie Roho Mtakatifu anishukie wakati namalizia tu. Kwanza nianze na lugha za kejeli, lugha za kuudhi.

Mheshimiwa Spika, sisi wengine ni vijana pia na bado hata umri wa busara haujafika, tuna hofu sana. Tunasihi, na mimi niseme tu kwa dhati, namuonya, aache lugha za kejeli ndani ya Bunge hili, aache lugha za kejeli ndani ya Bunge hili namuonya tu, hamna njuka hapa, njuka maana yake nini? kwa hiyo namuonya kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, lakini pia amezungumzia suala zima ya ATCL, unapotosha. Uchumi wowote duniani unapozungumzia usafirishaji inamaanisha kuwa ni huduma, it’s just a service, ni huduma tu, ku-facilitate maeneo mengine ya uchumi kama utalii, kilimo na maeneo mengine. Anakuja hapa anatudanganya, anadanganya Watanzania hapa tunampigia makofi hapa. Lugha za kuudhi nakuonya. (Makofi/Kicheko)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nichukue fursa hii kukushukuru, lakini pia nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyenipa afya njema hata siku ya leo nikawa sehemu ya wachangiaji kwenye Wizara hii muhimu kwa Taifa letu, Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Spika, naomba nianze mchango wangu kwenye eneo ambalo wananchi wa Jimbo la Mlimba wameniagiza niseme hapa halafu baadaye nitazungumza masuala ya kitaifa. Wananchi wa Jimbo la Mlimba wameniagiza nizungumze mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Spika, hoja kuu ni mgawanyo wa miundombinu ya huduma ya afya na elimu kitaifa. Tuna changamoto kubwa sana juu ya mgawanyo wa huduma hizi za elimu na afya kitaifa. Ni kweli hakuna ubishi Wizara hii hasa Serikali ya Awamu ya Tano imefanya kazi kubwa katika ujenzi wa vituo vya afya na kazi kubwa katika ujenzi wa miundombinu ya sekta ya elimu.

Hata hivyo, swali langu la msingi tufanye tathmini ya kina kitaifa tuone mgawanyo wa huduma hizi, wapo baadhi ya wananchi ukizungumzia habari ya huduma ya afya, ukiwaeleza takwimu ya ujenzi wa vituo vya afya hawaelewi lugha hii. Kwa sababu katika Jimbo zima, mfano naomba nizungumzie Jimbo la Mlimba, jimbo hili lina kata 16, vituo vya afya ni viwili tu. Uzuri wananchi wa Jimbo la Mlimba ni wachapa kazi na kauli mbiu yetu Jimbo la Mlimba ni “tunaanza wenyewe Serikali itatukuta”. Sasa tunaomba kuungwa mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mpaka sasa tumeshakamilisha ujenzi wa kituo cha afya, jengo la wagonjwa wa nje (OPD) na Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI dada yangu Ummy, maombi ya wana Mlimba tunataka tuanze kufungua kile kituo cha afya, tafadhali Mheshimiwa Waziri atuletee Waganga pamoja na wahudumu ili tuanze kufungua.

Mheshimiwa Spika, pia ikimpendeza Mheshimiwa Waziri anavyokuja kuhitimisha bajeti yake siyo mbaya akasema anakwenda kukamilisha kituo kile cha afya. Maadam tumeanza na siku zote unavyotaka kusafiri unaanza kukaa barabarani ndiyo unaomba lift. Kwa hiyo sisi tunaomba lift tusaidie tu tumalizie kituo cha afya.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la hii hii sekta ya afya, kwa wahudumu, hebu tufanye tathmini Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI, wapo wanaopewa nafasi hizi kwenye ngazi za Halmashauri hawana sifa, sasa tufanye tathmini ya kina halmashauri kwa halmashauri kama kuna mtu anayeshughulika na let’s say Mkuu wa Kituo cha Afya au Mganga Mkuu wa kituo cha afya tuone elimu yake, hebu tufanye tathmini ya kina kitaifa tuone kwa sababu sekta hii ni muhimu na nyeti sana.

Mheshimiwa Spika, labda nieleze tu ikama ya sekta ya afya ndani ya Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, mahitaji ni watumishi takriban 432 waliopo kwa sasa ni 169 unaona disaster hiyo, yaani zaidi ya nusu hawapatikani. Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri atusaidie katika eneo hilo na wananchi wa Mlimba wamenituma hayo.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine niende kwenye suala zima la sekta ya afya kuhusu maboma. Tumeshajenga sisi Mlimba maboma 10 ya zahanati. Tunaomba tumalizie tu, kama tunaanza wenyewe siyo mbaya tukaungwa mkono na Serikali.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo la elimu; kwa Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, nitoe tu mfano mathalani elimu ya msingi, mpaka sasa tuna maboma ya madarasa 41. Ushauri wangu hapa kama wametuletea fedha kujenga madarasa, watu wa Mlimba tunaomba sana zile fedha waturuhusu hata kama kwa ajili ya kujenga shule au madarasa tuzitumie kukamilisha maboma haya kwanza, watusaidie sana.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine, ikama ya Walimu wa elimu ya msingi. Mahitaji ni Walimu 1,420, waliopo ni 654 maana yake tuna upungufu wa Walimu takriban 766. Sasa tungeomba maeneo haya yatiliwe mkazo kidogo kwa sababu ni maeneo nyeti sana na kwa mustakabali wa watoto wetu na wanafunzi wanaosoma ndani ya Jimbo la Mlimba.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine niende upande wa TARURA; yapo mengi yamezungumzwa kuhusu TARURA. Mimi binafsi niseme tu, kwangu Jimbo la Mlimba mnyonge mnyongeni haki yake mpeni na nimwombe Mheshimiwa Waziri, watumishi hawa asiwahamishe ndani ya Jimbo la Mlimba. Meneja wa TARURA Wilaya ya Kilombero kwa maana ya Mlimba super, aniachie tufanye naye kazi. Meneja wa TARURA Mkoa wa Morogoro super, tauachie tufanye nao kazi. Nitasema baadaye huko kwenye maji maana yake wako wazuri zaidi kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye eneo la mgawanyo wa fedha hizi za TARURA. Nilikuwa najaribu kuangalia haraka haraka Jimbo la Mlimba lina kilometa zaidi ya 1,000, tunapata bajeti ya milioni 500 kwa mwaka. Nimeangalia na jirani zangu pale Kilosa kidogo, wao wana kilometa takriban 900 hivi wana bilioni 1.3. Sasa napata tabu kwenye mgawanyo wa hizi fedha, milioni 500 unafanyia nini pale Mlimba, kilometa zaidi 1000. Yaani hata daraja moja halikamiliki. Hebu tuangalie maeneo haya, niombe tu na nimwombe Mheshimiwa Waziri wakati anakuja kuhitimisha bajeti yake aeleze ni vigezo gani vinatumika katika mgawanyo wa hizi fedha kwenye halmashauri, nivijue vizuri. Hii itatusaidia pia kupata elimu.

Mheshimiwa Spika, sasa nijikite katika eneo la mapato na hapo kwanza natangaza maslahi na kwa kuwa nimehudumu kwenye Serikali za Mitaa kama Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma na tulifanya vizuri sana kwenye mapato, naomba nitoe elimu kidogo kwa ufupi kwenye eneo hili.

Mheshimiwa Spika, hakuna muujiza kwenye kuziimarisha halmashauri kimapato, jambo la msingi niombe Wizara hebu tufanye tathmini, tuangalie fursa za kila halmashauri, nilivyokuwa Dodoma niliitazama Dodoma Jiji nikaona sina fursa nyingine mbadala zaidi ya ardhi, tukapima Dodoma zaidi ya viwanja 200,000 tukapata fedha na tulikusanya bilioni karibu 73 kwa mwaka wa fedha 2018/2019. Tukasema hapana hii fedha viwanja siyo sustainable yaani sustainability ya mapato ya viwanja ni ya muda mfupi tu, nikakaa na menejimenti timu yangu tukakubaliana tubuni vyanzo mbadala vya mapato ya ndani, leo tumeacha hoteli kubwa hapa inayojengwa kwa mapato ya ndani bilioni 9.9 inakamilika, ndiyo tunafungua mwezi ujao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Jiji la Dodoma kwa maana ya own source ipo. Ukienda Mji wa Serikali kuna hoteli, kuna apartment, kuna kumbi zinajengwa, mapato ya ndani bilioni 18. Sasa niombe na niseme tu zipo halmashauri zina fursa ya kilimo, wawekeze kwenye kilimo, zipo halmashauri zina fursa kwenye maeneo mengine wawekeze huko, hakuna eneo ambalo halmashauri tunazuiliwa kwa mujibu wa sheria kuwekeza. Tukiendelea kusubiri haya sijui kodi na nini nadhani tuta-mark time kidogo.

Kwa hiyo niombe na sisi pale Mlimba waturuhusu nitamwomba Waziri wa Ardhi baadaye lakini kwa sababu hapa tunazungumza na TAMISEMI, kuna shamba la Serikali la hekta 500 limetelekezwa leo hii almost ni miaka kama mitatu, sisi tutalichukua lile na tutalima kuanzia mwakani. Tutaanza kilimo cha mpunga, tuvune mpunga kama mapato ya ndani, tutalichukua tu sisi maana Serikali haifanyi chochote pale. Kama halmashauri tutalitumia, tutaliwekeza ili tulime kilimo cha mpunga, tuone namna gani tuweze kujikwamua na shughuli za maendeleo Jimbo la Mlimba kupitia kilimo cha mpunga.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, naomba niseme jambo moja tutengeneze clusters ya hizi halmashauri. Huwezi kulinganisha Jiji la Dar es Salaam kwa maana Ilala na Halmashauri ya Mlimba hata kidogo. Kwa hiyo hata fedha za maendeleo tunavyopeleka tuzitengenezee madaraja. Daraja A ni halmashauri zile zote zenye uwezo kwa mapato ya ndani, tuangalie namna gani tunapeleka kwa sababu ukisema mgao wa Ilala uwe sawa na wa Mlimba, tunawaonea haziwezi kuwa sawasawa. Kwa hiyo tuzitengenezee madaraja, kama hawa wana uwezo wa mapato ya ndani, basi ziende fedha chache za maendeleo, wale wenye changamoto kubwa tuwapelekee za kutosha na hili ni tatizo la nchi nzima. Ilala ana zaidi ya bilioni 60 unampelekea fedha za nini, Dodoma Jiji sasa wanakwenda kukusanya bilioni 48, sisemi zinatosha lakini tuangalie namna ya mgawanyo kwa kuzingatia fursa au uwezo wa halmashauri kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, eneo la mwisho ambalo nadhani nitoe mchango wangu ni 10%. Sheria imetungwa na nalipongeza sana Bunge lililopita na nakupongeza na wewe binafsi kwa sababu mlitunga sheria nzuri sana. Tuweke eneo kwenye kanuni au sheria, nadhani kanuni kwenye utekelezaji kwa sababu kanuni ndiyo inatekeleza sheria. Tuweke eneo ambalo halmashauri zenye uwezo mkubwa wa kuchangia 10% zisipeleke fedha kwa sababu tija zile hela tunapopeleka kwa wananchi hazifanyi chochote, tunafanya siasa tu. Dodoma sasa hivi tumepeleka bilioni sita, ziko mtaani, hebu fanya tathmini hizo bilioni sita zimefanya nini? Utaona hamna kitu kwa hiyo kama ni siasa tu. Kwa hiyo halmashauri zenye uwezo wa fedha nyingi ziruhusiwe badala ya kupeleka fedha watengenezewe shughuli yoyote kiuchumi yaani halmashauri iamue kununua kama ni vifaa au namna gani yoyote lakini siyo kupeleka.

Mheshimiwa Spika, kingine kuwe na ukomo wa hizi fedha, leo hii Dodoma kama inatoa zaidi ya bilioni sita, maana yake itafika mahala 10% ni zaidi ya bajeti yake tunapeleka kwa wananchi, kwa hiyo kuwe na ukomo kwa halmashauri kubwa kwamba sasa ifikie mahali kama utachangia 10% mpaka bilioni 30 i-stop, zile changa ziendelee kwa sababu wakati inatungwa sheria hii hatukutathmini kwa kina uwezo wa halmashauri husika.

Mheshimiwa Spika, kwa haya machache niliyochangia, nadhani yatasaidia Wizara yetu, lakini nimwombe anapokuja kuhitimisha bajeti yake, haya niliyomwomba ayaseme na niyasikie na wananchi wa Mlimba roho zao zitapona. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 –Wizara ya Katiba na Sheria
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, Nikushukuru kwa dhati kabisa lakini niipongeze Wizara hii ya Katiba na Sheria ina Waziri mahiri kabisa, mbobezi wa masuala ya sheria.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze mchango wangu kidogo nikumbushe jambo kama binadamu. Katika jambo ambalo ni gumu na linahitaji umakini mkubwa kwenye maamuzi ni suala la utoaji wa haki. Nadhani kama unafanya ranking, suala la utoaji wa haki linashika number one duniani; kwasababu ni jambo ambalo mungu ameamini mamlaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna Sheria hizi mbili ya Utakatishaji wa Fedha na Uhujumu Uchumi, Bunge letu Tukufu lilitunga hizi sheria kwa nia njema kabisa; changamoto inayotukuta sasa ni utekelezaji wa sheria hizi. Naomba nikumbushe, wanadamu hapa duniani kwa Mujibu wa Biblia kizazi chetu ni cha nne, na uhai wetu hapa duniani ni miaka 70 hakuna anayeishi hapa milele.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa sitaki kujua umri wa kila mmoja kila mmoja anaweza kutafakari aangalie miaka 70 a-minus umri wake sasa aone kipande alichobaki nacho duniani. Mtume Paulo kwa Habari ya Wakorinto aliwaeleza habari hii, aliwaeleza kwamba nikiitazama dunia ni ubatili mtupu. Hapa duniani tuwe na mali, fedha na kila kitu ni ubatili mtupu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali. Ofisi hii kama ni chakula ndio mpishi, akikosea huyu hii haki pale haitendeki na akipatia haki inatendeka.

Mheshimiwa Naibu Spika kuna jambo moja la ajabu sana limetokea pale jimboni kwangu yamkini ni kweli wananchi wale wamefanya makosa, vifaa vyao matreka yamekutwa kwenye hifadhi na inasadikika kwamba wamekutwa wakifanya shughuli za kilimo kwenye hifadhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii wananchi hawa wapo mahabusu na kesi walizonazo ni Uhujumu Uchumi ni jambo la kushangaza kweli! Jambo la kushangaza kweli! Duniani kwamba kuna jambo linalohitaji umakini narudia kusema, ni jambo la utoaji wa haki. Kama mwanadamu akionewa, kama alitenda kosa mungu ametuumba lakini ndio guilty conscious yaani kuna adhabu ukipewa na umetenda nafsi yako hata kama hutasema inasema kweli nilikosea, nafsi inasema. Lakini ukionewa nafsi ina masikitiko na manung’uniko hakika aliyefanya makosa haya anachangamoto.

Mheshimiwa Naibu Spika, manung’uniko ya wanadamu mungu anasikia; leo hii kuna watoto, wake, Mheshimiwa Waziri, wake, watoto; hawasomi walikutwa tu kwenye hifadhi, matrekta hayo wanalima uhujumu uchumi, eeeh! Tumefika hapo! Kwa hiyo, ofisi ya DPP tusaidie, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali tusaidie.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nimekuwa kiongozi wa taasisi tena kubwa tu; ukiwa kiongozi wa Jiji la Dodoma tena nafasi ya Mkurugenzi ni nafasi kubwa ya juu. Sasa nataka kusema nini? Kuna umakini mkubwa unatakiwa kwenye ushauri wa wasaidizi wetu kama husomi documents aaah! Unaletelewa tu, kuna wengine wana compromise rushwa huko, wameshindwa kupata rushwa anasema ngoja nimkomeshe huyu anakuletea na wewe unakubali. Kwa hiyo kuna jambo la umakini sana Ofisi ya DPP tusaidie. Watanzania wanalalamika, watanzania wananung’unika hasa wananchi wa Jimbo la Mlimba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Mheshimiwa Waziri na yeye binafsi alifuatilie, kama ikisadikika wananchi ni kweli wana makosa sheria ichukue mkondo wake. Mimi nishauri, Mheshimiwa Waziri ikikupendeza usiende tu kutembelea magereza nenda kalale! Usiende kutembelea kama visitor, nenda kalale, amka asubuhi utaona habari ya kule ndani. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kama kuna jambo gumu ni magereza. Ukimpeleka mwanadamu kule hana hatia kilio na masikitiko yake hutabaki salama. Kwa hiyo, naomba tuwe na umakini mkubwa katika suala zima la utoaji wa haki. Sheria hazina makosa, makosa ni namna ya utekelezaji wa sheria. Narudia kusema Ofisi ya Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali, tafadhali!

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye Mabaraza ya Ardhi. Yameelezwa hapa na Kamati imeshauri…

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa hebu weka vizuri hiyo sehemu ili tuwasaidie hata upande wa Serikali inapokuja kujibu hoja. Katika maelezo yako nilikuwa najaribu kufuatilia nijue unaelekea wapi lakini umeeleza kwamba matrekta yamekutwa kwenye hifadhi.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Naam!

NAIBU SPIKA: Ni uhalisia kwamba yamekutwa huko?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Sasa hayo ndiyo yanayoelezwa kwenye ile…

MBUNGE FULANI: Charge sheet.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Not charge sheet, nilipitia taarifa ya DPP, pamoja na mambo mengine kwenye facts alikuwa akitoa taarifa…

NAIBU SPIKA: Sawa.

Waheshimiwa Wabunge, ndiyo maana nilieleza mwanzoni yale mambo yaliyoko kule ukiyaleta hapa na sisi hatunayo unatupa wakati mgumu sana. Hata Serikali ukitaka ikujibu itakujibu kwenye hoja ipi? Kwa sababu katika maelezo yako wewe mwenyewe unayewatetea wale watu walioko ndani unasema hivi; wamekutwa na matrekta kule kwenye hifadhi. Sasa kama amekutwa na trekta kwenye hifadhi, lile trekta kwenye hifadhi linafanya nini?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika.

NAIBU SPIKA: Ngoja, ngoja, nakuelezea hoja simaanishi uanze kujibizana. Ni hivi; ukiwa na jambo mahsusi waeleze wakalifuatilie. Ukilieleza wewe kwa namna ya kwamba na wewe unalifahamu kwa kadri Ofisi ya DPP inavyofahamu, Serikali inavyofahamu utapata wakati mgumu ndiyo maana hata hapa umeanza kusema ndicho walichoeleza maana yake ndicho walichoeleza Serikali lakini watu wako wewe walikutwa kule au hapana? Rekodi za Bunge hapa zitaonesha kwamba Mbunge umesema walikutwa na matrekta kule kwenye hifadhi.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Nimesema inasadikika.

NAIBU SPIKA: Mimi nilikuwa nasikiliza na huwa nasikiliza kila neno ndiyo maana nakueleza. Sasa mchango kama huo ukibaki hapa halafu wale wakaamua kwamba ni ushahidi Mbunge wenu mwenyewe alisema kwamba imekutwa kule. Kwa hiyo, ndiyo maana huwa najaribu kuonesha kwamba tuchangie kwa namna ambayo unaieleza hoja hiyo kwamba Serikali ikafuatilie. Taarifa za ziada waache wao watazipata na wewe kama Mbunge ni haki yako kabisa kwenda kwenye ofisi ya DPP, kwenda kwa Waziri kumueleza watu wangu wako kule hawajafanya kosa ama kwa namna yoyote ile unayotaka kuwatetetea. Ukiiweka humu kwa mtindo huo inaonekana kwamba katika taarifa rasmi na wewe unasema wamekutwa kule. Mimi nilikuwa nasikiliza kwa makini kabisa.

Nenda kwenye hoja yako ya pili, hii ya kwanza nakushauri uonane na DPP kwa sababu ofisi yake iko wazi Mheshimiwa Waziri pia yuko hapa. Karibu sana umalizie mchango wako.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, nashukuru kwa ufafanuzi na kama Hansard iko sawasawa nimetumia neno inasadikika.

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye eneo hili la Mabaraza ya Ardhi. Mengi yameelezwa hapa kwa habari ya Mabaraza ya Ardhi kwamba yawe sehemu ya Mahakama. Mimi nitakuwa na mchango wa tofauti kidogo, isingefaa Mabaraza haya yawe sehemu ya Mahakama isipokuwa Mheshimiwa Waziri wa Katiba na Sheria atusaidie kama kuna eneo kwa mujibu wa Kanuni kwenye ile sheria iliyoanzisha Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya liongezwe kabla hajatoa maamuzi Mwenyekiti wa Baraza ni lazima athibitishe kwamba amefika eneo la tukio.

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto inayojitokeza kwenye haya Mabaraza kwenye utoaji wa hati unakuta Mwenyekiti wa Baraza anajifungia kwenye chumba anatoa maamuzi na mgogoro wa ardhi ni lazima ufike eneo la tukio, ndiyo changamoto hiyo tu. Kwa bahati mbaya ukienda Mahakama Kuu inayoshughulika na masuala ya ardhi, haina nafasi ya kukusanya ushahidi. Kwa hiyo, hata maamuzi ya Mahakama Kuu ukimueleza mlalamikaji au mlalamikiwa, mdai au mdaiwa akate rufaa Mahakama Kuu haina nafasi tena ya kukusanya ushahidi. Kwa hiyo, matokeo yake huyu mtu atendewe haki tu, hata rufaa bado ni changamoto tu. Kwa hiyo, msingi wa jambo lenyewe ni pale linaposikilizwa kwa mara ya kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Wenyeviti wa Mabaraza ya Ardhi na sasa hivi inakuwa ni utashi tu tena mlalamikaji anaambiwa nipe fedha ya kwenda site, Mtanzania wa kawaida hana. Sasa namna gani haki inatendeka, changamoto iko hapo. Kwa hiyo, ushauri wangu kwa mujibu wa Kanuni au sheria yenyewe kuwe na eneo linalosema kwamba kabla hajafanya maamuzi ya mwisho ahakikishe amefika eneo la tukio. Ndiyo essence ya migogoro ya ardhi.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nikushukuru kwa dhati na Mwenyezi Mungu akubariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu aliyeniwezesha wakati wa asubuhi najiandaa kuja kuchangia Wizara hii muhimu, nilimwomba Roho Mtakatifu anipe hekima na busara nichangie Wizara hii muhimu kwa maslahi mapana ya Taifa letu Tanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, nitajielekeza kwenye maeneo yafuatayo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la kwanza ni eneo la upangaji, upimaji na umilikishaji; Eneo la pili ni changamoto za sekta ya ardhi; Eneo la tatu ni ushiriki wa sekta binafsi; Eneo la nne ni mashamba yasiyoendelezwa; na eneo la tano muda ukiruhusu, ni Mabaraza ya Ardhi na mwisho nitahitimisha na Shirika la Nyumba.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la upangaji, upimaji na umilikishaji; labda nirejee historia kidogo. Mnamo mwaka 1896, kiwanja cha kwanza kilipimwa nchini wakati wa Mkoloni. Hali kadhalika, tangu Uhuru mpaka leo, upangaji ni viwanja milioni sita.

Mheshimiwa Naibu Spika, ninavyosema upangaji, ni hesabu ya viwanja kwenye ramani za mipango miji katika mchakato wa uandaaji wa kiwanja. Ukipima hivyo milioni sita kwa mujibu wa utaalam, unaweza ukajikuta huwezi kupata milioni sita vyote vitapungua kwa sababu ya mokorongo na maeneo ambayo ni hazardous areas.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni upimaji wa viwanja. Viwanja vilivyopimwa tangu Uhuru ni milioni mbili na laki tano tu na viwanja vilivyotolewa umiliki ni takribani milioni moja na laki tano tu. Nilikuwa najaribu kuwasiliana na wenzetu wa Kenya, wenzetu sisi tunasema upangaji viwanja milioni sita, Kenya milioni sita ni hati miliki; mnaona kuna tofauti kidogo. Kwa hiyo nataka kujenga hoja ya namna gani hapa; hoja yangu ya msingi hapa ni kasi ndogo ya upimaji, upangaji na utoaji wa hati nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa nijielekeze kwenye ushauri; nitaeleza baadaye kwenye hoja hiyo ya namna gani sasa tunaweza kuongeza uwezo wa upimaji, upangaji na upatikanaji wa hati nyingi sana kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende eneo la pili, kwa sababu ya muda naongea haraka haraka kidogo ila kuna pointi muhimu nitaongeza kidogo maelezo. Niende kwenye eneo la changamoto za sekta ya ardhi. Changamoto za sekta ya ardhi nchini ni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya kwanza ni gharama za umilikishaji. Mheshimiwa Waziri atakumbuka alikuwa ukipiga simu kuwataka wananchi waje wachukue hati. Unajua changamoto kubwa inayotukuta ni nini? Kuna gharama inaitwa tozo ya premium, tozo ya mbele, hii gharama ni kubwa. Kwa hiyo wananchi wengi, hasa wa kipato cha chini, wanashindwa kumudu gharama hizi. Kimsingi, tukiziondoa gharama hizi za premium, na Waziri yupo hapa, mjamba wangu, Mheshimiwa Lukuvi, namwambia kwa dhati mwamko wa wananchi kutaka kupata hati utakuwa mkubwa sana na watajitoa kulipia kodi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine la changamoto ni ukosefu wa kanzidata ya uhakika ya hati miliki za viwanja. Leo hii nina uhakika mjomba wangu hapa Waziri Mheshimiwa Lukuvi nikimuuliza anieleze takwimu sahihi ya viwanja vilivyopimwa nchini kidogo kutakuwa na mtihani. Kwa hiyo nishauri Wizara, sasa tuanzishe kanzidata na zaidi teknolojia imekua, tuweke mfumo tu wa teknolojia, watu waweze kujua na mtu yeyote nchini aweze kujua na kila mtu awe na access ya kujua, kwa hiyo ni jambo dogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, niendelee eneo lingine la uhaba wa watumishi; ni kweli changamoto kubwa Sekta ya Ardhi kama nitakosea Surveyors hawazidi 600 wa Wizara ambao ukiwachukua na wale wa kwenye halmashauri. Maafisa Ardhi hawazidi takribani labda 2,000 na kidogo. Sasa nchi nzima unaona namna gani kuna huu uhaba wa watumishi.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimwombe Waziri na niombe Wizara ya Fedha pia, ione namna ya kuona kutatua kero hii ya watumishi. Pia, leo hii Wizara ya Ardhi imehamisha watumishi kutoka Mamlaka ya Serikali za Mitaa yaani TAMISEMI kwenda Wizara ya Ardhi tuwatengenezee utaratibu bora watumishi wale.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii ukienda kwenye mikoa hawana vitendea kazi, utamwambia Kamishna wa Ardhi aende kwenye halmashauri hana gari ataendaje? tutawezeshe ili wafanye kazi nzuri. Pia natarajia kuona hata kwenye wilaya tupeleke vitendea kazi ili kusudi hii kazi iendelee vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende eneo lingine la uwezeshaji mdogo wa shughuli za Sekta ya Ardhi; nishukuru sana, sasa nimeona kuna mabadiliko na niseme kwa dhati kitendo cha Serikali kuanza ku-finance halmashauri ni wazo jema sana, lakini fedha bado ndogo, ndogo sana. Sasa nitoe tu ushauri wangu Wizara ya Fedha tuki-finance Wizara ya Ardhi itatusaidia kupata pato la kutosha kabisa na nitaeleza baadaye namna gani tunaweza kupata fedha hizo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nijielekeze katika migogoro ya ardhi; unajua migogoro ya ardhi ikiwa mingi ni miongoni mwa indicator za failure ya Wizara. Kwa hiyo namwomba mjomba wangu suala hili la migogoro ajitahidi tulimalize kwa kutumia Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya hadi Wenyeviti wa Vijiji kule kwenye ngazi ya wilaya, wafanye kazi hiyo vizuri, ili awe Mamlaka ya Rufaa tu, kwenda kwenye kijiji, ataenda vijiji vingapi, kwa hiyo tuwaachie wale wafanye kazi hiyo kwa uhakika zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende eneo lingine la ushiriki wa Sekta Binafsi; hapa naomba nijielekeze kwenye makampuni ya upimaji. Hapa nitulie kidogo, mimi nina success story hapa ya Dodoma, nazungumzia Mbeya na wapi, jamani mbona Dodoma hamsemi, Dodoma hata hela haikupewa imefanya maajabu hapa na sisi tunakaa hapa. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana tu Manispaa ya Dodoma ilivyokabidhiwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu yaani CDA, tulikabidhiwa Mamlaka ile na deni la bilioni 12 na fedha kwenye akaunti ya milioni 400 tukapewa maelekezo na Serikali tupime watumishi wapate viwanja, hatuna fedha, mimi ndiyo nilikuwa Mtendaji Mkuu kama Mkurugenzi wa Manispaa by then. Tulichokifanya tukashauriana ndani ya Jiji la Dodoma tukasema tukitumia watumishi wetu hawa ambao wapo wachache hatuwezi kufanikiwa, tukaalika Sekta Binafsi, mimi nilifanya majaribio, nilitumia pale Michese viwanja 2,000 nikapeleka watumishi wangu wa halmashauri waliniletea vile viwanja baada ya miaka mitatu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hizi fedha tunazoweka kwenye halmashauri tuwaachie wasimame wenyewe bila Sekta Binafsi tunakwenda kufeli asubuhi kweupe. Sekta Binafsi nilivyo-engage makampuni haya yametusaidia Dodoma tukapima viwanja 200,000; sikupata fedha Serikali Kuu, sikwenda kukopa mkopo benki, hii ni success story tukitaka kujifunza tusiende Ulaya mje Dodoma hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, unajua wakati mwingine huwa tunaamini ngozi nyeupe, Kunambi ningekuwa ngozi nyeupe hapa wangeamini, sasa kwa sababu ni Mtanzania huwa hatutaki, lakini tujifunze tu na sisi ni wadau, kwa sababu tuna uwezo wa kufanya maajabu ndani ya Taifa hili. Kwa hiyo Dodoma ni success story na nadhani Wizara ya Ardhi wachukue kama model.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nimpongeze Waziri juu ya suala la mfumo ILMIS - Integrated Land Management Information System. Kengele?

MBUNGE FULANI: Bado.

GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa mfumo ule, kwa sababu ukienda Dar es Salaam kuna mafanikio, ameuleta Dodoma na nimwambie kwa dhati, Dodoma viwanja hivi 200,000 vinaenda kupata hati kupitia ule mfumo, nampongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ombi langu Mheshimiwa Waziri ule mfumo sasa aupeleke kwenye halmashauri zote nchini, kwa sababu gharama ya ule mfumo Mheshimiwa Waziri, Afisa Ardhi mmoja anaweza akatengeneza hati 300 kwa siku. Kwa hiyo kwa sababu ya uhaba wa watumishi tulionao, ukimtumia Afisa Ardhi mmoja ukampa server, akawa integrated akawa na communication na Kamishna na Msajili kule na ana computer yake, ana-server na printer, yeye kazi yake ni kubofya tu taa, hati 300 zinatoka. Leo hii tunatengeneza hati bila mchapa hati yule anachapa hati 10 kwa siku, tutafika 200,000 kweli hapa Dodoma. Kwa hiyo, niishauri Wizara kwa dhati kabisa katika eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende kwenye eneo la mashamba yasiyoendelezwa, pale jimboni kwangu Mlimba kuna Shamba la Kambenga ekari 1,000 hazijaendelezwa Serikali ipo. Pale Mlimba kuna Shamba la Serikali hekta 5,000 Kata ya Mgeta hazijaendelezwa, mwaka wa tano Serikali ipo. Kuna Shamba la Balali ekari 2,000 halijaendelezwa lipo. Waziri anapokuja kuhitimisha hapa bajeti yake anieleze mjomba wangu kwa dhati nini mpango sasa wa Wizara kwenda kuyaondoa mashamba darasa haya ili wananchi wa Mlimba wapate maeneo na mashamba walime.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine niende haraka haraka, ni eneo hili na kwa dhati kabisa juu ya Mabaraza ya Ardhi, ukienda kwenye level ya Mabaraza ya Kata wale siyo Wanasheria na bahati nzuri uliyekalia kiti wewe ni Mwanasheria utanisaidia kwenye eneo hili, wale hawapaswi kutoa maamuzi kwa sababu bahati mbaya zaidi maamuzi yao yale yanakuwa ni rufaa kwenye Mabaraza ya Wilaya. Ushauri wangu wawe wasuluhishi tu, wale wanaosuluhishana wakishindana basi rufaa iende kwenye Baraza la Ardhi la Nyumba na Wilaya ndiyo lifanye maamuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, kwa dhati kabisa niombe, Mungu atubariki sote. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Kilimo
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa fursa hii muhimu, nianze kwa kuipongeza Wizara.

Mheshimiwa Spika, wakati umenitaja nichangie nilikuwa naangalia viongozi wakuu wa hii Wizara. Nimetazama Waziri naona ni Profesa, nimetazama pia nafahamu kaka yangu Bashe yeye ana Masters lakini namuona pia Katibu Mkuu yeye naye bila shaka ana Masters lakini pia kuna Prof. Siza.

Mheshimiwa Spika, normally people they do not care about how much you know until you know about how much you care. Naomba nirudie normally people they do not care about how much you know until you know about how much you care. Telling people, you are a professor/Ph.D holder/ Masters’ holder is nonsense if you don’t deliver services to the society. Kuwaeleza watu kwamba mimi ni profesa, daktari, nina masters kama hutoi huduma kwa jamii ni kazi bure. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, changamoto sio weledi, sina mashaka na weledi wa viongozi wa wizara hii ni mahiri kabisa kwa maana ya knowledge. Changamoto kubwa niliwahi kusema hapa na hii ni kwa Watanzania tulio wengi ni mambo matatu; la kwanza ni mtazamo (mindset), la pili ni commitment na ya tatu ni uzalendo basi, sio fedha. Tunazungumza financing, kwenye kilimo hakuna. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme neno moja, nchi za Ulaya karne ya 16 zilianza mapinduzi ya kilimo (agrarian revolution) ndiyo wakaenda kwenye viwanda, walivyotoka kwenye mapinduzi ya kilimo wakaenda kwenye mapinduzi ya viwanda karne ya 18. Na walifanikiwa tu baada ku- engage private sector, kazi ya Serikali tusi-engage pia na kwenye masuala… kazi moja tu nishauri Wizara tuandae mashamba mazuri yaliyopimwa vizuri, tutafute private sector tuwaambie tunawakabidhi haya; ukienda Zambia wanafanya hivyo na nchi zote zilizofanikiwa kwenye kilimo wanafanya hivyo.

Mheshimiwa Spika, leo hii hata tukisema hapa bajeti ya Wizara ya Kilimo iongezwe kutoka asilimia 0.8 hiyo fedha unatoa wapi, haipo; turuhusu sekta binafsi. Kazi ya Wizara iwe ni namna ya usimamizi…

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Pokea taarifa Mheshimiwa Godwin.

T A A R I F A

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante, naomba nimpe taarifa mzungumzaji kwanza anachochangia ni sahihi sana na kimsingi sio kwamba tutafute private investors kwenye ishu ya kilimo, wapo vijana ambao wanafanya vizuri ambao hata Wizara ni mashahidi na watu wa SUA ni mashahidi. Vijana kama Malembo Farm ambao wanafanya consultation, RAYMAK wapo Miyuji tu hapa Dodoma ambapo pia Wabunge wanaweza kwenda pale kuona RAYMAK yupo pale anafanya agribusiness. Kwa hiyo, wapo vijana ambao wameshajitolea kufanya hiki na wanafanya mpaka greenhouse, wanafanya vitu vikubwa sana. Kwa hiyo, tunaweza tukaanza na hao kuwapa hata ruzuku waendelee kufanya shughuli zao, ahsante. (Makofi)

SPIKA: Unaipokea hiyo taarifa Mheshimiwa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nadhani anaendelea kuniunga mkono.

Mheshimiwa Spika, niendelee kusema tu kwamba lakini pia financing agriculture, tutafute benki ambazo zisikae Dar es Salaam, Dodoma wala zisikae mijini ziende kwenye maeneo ya kilimo. Yaani mkulima anaweza kukopa benki iwe kwenye Kata yake. Leo hii ukimwambia mkulima kuna benki zinazo-finance kilimo hawajui, hawajui kabisa. Kwa hiyo, twende kwenye private sector kama nilivyosema awali tutenge maeneo maalu, lile shamba lipimwe liwe na hati mkulima anaweza kukopesheka. Kwa hiyo, Wizara hizi zishirikiane; Wizara ya Kilimo, Wizara ya Ardhi na Wizara ya Viwanda wafanye kazi kama timu moja. Naamini tunakwenda kufanya mapinduzi makubwa ya kilimo ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, nijikite kwenye eneo hili la zao la mpunga; tumekuwa tukizungumzia mahindi. Duniani kote chakula kinacholiwa na watu walio wengi ni mchele kwa maana ya mpunga, sio mahindi, mahindi wakati mwingine Marekani wanakula Wanyama lakini mpunga/mchele wanakula wanadamu duniani kote, ukienda Japan wapi. Sasa zao la mpunga leo hii ukiuliza soko la mpunga na hii niiseme nisije nikasahau wakati Mheshimiwa Waziri unakwenda kuhitimisha bajeti yako nisaidie umejipangaje hasa kwenye soko la zao la mpunga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jimbo langu nalima zao la mpunga kwa maana ya Mkoa wa Morogoro ukiondoa wenzetu wa Mbarali na Kyela, Jimbo la Mlimba tunashika nafasi ya tatu kwa kilimo cha zao la mpunga lakini wananchi wangu mpaka leo. Mwenyewe nimefungia gunia 70 ndani sina mteja. Sasa na mimi mkulima pia, nataka ni-declare interest hapa. Kwa hiyo, nimefunga mpunga wangu upo ndani sina mteja wa kuuza, Mbunge sina je wananchi wangu ikoje? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, itoshe kusema tusijikite kwenye mahindi ambayo wakati mwingine yana alternative, mpunga hauna alternative. Kwa hiyo, tutafute masoko kwenye zao, hata maghala huwezi kuona ghala la mpunga; lipo ghala la zao la mpunga, hamna hata maghala tu. Kwa hiyo, zao hili ni muhimu sana.

Mheshimiwa Spika, nirudi tu moja kwa moja nijikite kwa wananchi wangu wa Jimbo la Mlimba ambao wamenituma nifanye kazi hii. Pale Kata ya Mngeka kuna shamba la Serikali la hekta 5,000. Shamba hili hekta 3,000 tayari zina miundombinu ya umwagiliaji lakini huu ni mwaka wa nne shamba lile Serikali imelitelekeza; leo tunasema irrigation scheme iko pale hatuitumii.

Mheshimiwa Spika, namshukuru Wizara ya Fedha imeanza kuchukua hatua, kulikuwa kuna deni la NMB kuna mwekezaji uchwara alienda pale sijui akafanya nini akaondoka akaacha deni kama bilioni 10, jana Mheshimiwa Waziri wa Fedha amenipa matumaini amesema sasa wamechukua jitihada wanakwenda kulipa lile deni lakini changamoto hizi hekta 5,000 zinakwenda kufanya nini.

Mheshimiwa Spika, wananchi wa Mlimba miaka ya 1985 wakati Hayati Baba wa Taifa amepata msaada wa nchi ya Korea ili nchi yetu ijikimu katika chakula, alipata msaada huo Wakorea wakaja wakajenga mitambo kila kitu hadi umeme tunafua pale wenyewe megawatt karibu 350 tunatoa pale ile mitambo iko pale kama park elephant.

Mheshimiwa Spika, sasa nikanasema namshukuru Waziri wa Fedha, akishalipa hilo deni la NMB, hizo bilioni 10 msimu ujao kama Serikali haijatuletea mwekezaji pale nitawaambia wananchi wangu tukalime, hatuwezi tukaacha maeneo yanakaa tu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nitachukua hatua tu, nitaenda kuhamasisha wananchi wa Mlimba, tukalime hizo hekta 5,000 nadhani tutasimamiwa na Halmashauri yetu ya Mlimba.

T A A R I F A

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Mheshimiwa Musukuma.

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naomba kumpa taarifa mzungumzaji, niko Kamati ya Nishati na Madini sijawahi kusikia kama Mlimba tuna megawatt 350, kilowatt au megawatt ili kumbukumbu zikae sawa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, sipokei taarifa kwa sababu haihusiani na hoja ninayojenga hapa, naomba niendelee.

Mheshimiwa Spika, nataka kusema nini? Nazungumzia suala la zima la namna gani tunaweza kufanya kilimo chetu kiwe na tija, kwa mfano, tunaeleza kwa Habari ya asilimia 65 ya wakulima, na kule ukienda kijijini wako wazee tu sisi vijana wote tuko mijini kwanini kilimo hakituvutii kwa sababu Serikali haijaweka mazingira Rafiki kwa vijana kupenda kilimo. (Makofi)

MHE. ENG. AISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Na kwa bahati mbaya tunasema ajira, ajira!

SPIKA: Naona kuna taarifa nyingine tena endelea Mheshimiwa nimekuona.

T A A R I F A

MHE. ENG. AISHA N. ULENGE: Mheshimiwa Spika, naomba kumpa taarifa mzungumzaji kwamba anachosema ni kitu sahihi kuna daktari mmoja nchini Afrika ambaye ameishauri Wizara husika ya kilimo katika nchi yake kwamba kilimo kinapaswa kufanywa kuwa sexy ili vijana wakivutie. Huwezi kuweka kitabu cha kilimo kina picha cha bibi mzee amechokaa kijijini always haiwezi kum-attract kijana kujiunga kwenye kilimo. Let make the agricultural sector sexy to attract youth. (Makofi)

MHE. GODWNI E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, naipokea taarifa.

SPIKA: Unapokea taarifa hiyo Mheshimiwa Godwin?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, naomba niseme jambo moja niliwahi kupata fursa ya kwenda training ya quality ya infrastructure system kule Japan Tokyo. Nilipofika kule walikuwa wakisema wa Japan wale, wanaagiza chakula cha mwaka mzima kutoka nje ya nchi, ikiwemo nchi nyingi za Afrika, wanaitaja Zambia, wameitaja pia na Zimbabwe, why not Tanzania? Why not Tanzania hoja ndio kama hizi kwamba bado tuna changamoto kubwa hatujaweka mkazo mkubwa kwenye kilimo.

Mheshimiwa Spika, itoshe tu kusema kwamba tukiweza kuongeza thamani kwenye mazao ya kilimo itatusaidia ku-export na faida kwenye uchumi uki-export sana halafu leo hii cha ajabu zaidi tuna ardhi ya kutosha, tuna yenye rutuba, lakini bado tunaagiza mazao yanayotokana na kilimo nje ya nchi kwa mfano suala la sukari, leo hii sukari unaagiza nchi ya nje kuliko Tanzania kweli?

Mheshimiwa Spika, mimi nataka kusema tu kwamba hasara tunayoipata Watanzania kwa kuagiza sukari na ngano, wachumi watanisaidia kwenye uchumi kuna terminology tunasema capital flight ambapo ni kitendo cha kukusanya fedha za ndani ya nchi kwenda kubadilisha na dola kununua bidhaa nje ya nchi. Definitely, tutapata inflation ambayo inasababishwa na capital flight lakini tukizalisha kwa wingi mazao ya kilimo tutakuwa na balance of payment na nchi yetu ita-invest na kuwekeza kwenye maendeleo mengine ya uchumi.

Mheshimiwa Spika, wakati wa kupitisha bajeti ya Mheshimiwa Waziri naomba mambo mawili; jambo la kwanza anieleze ni lini skimu yangu ya umwangiliaji Udagaji inakwenda kuendelea, maana mpaka sasa imetelekezwa na shilingi milioni 30 imepelekwa pale.

Mheshimiwa Spika, jambo la la pili Mheshimiwa Waziri au kaka yangu Mheshimiwa Bashe Naibu Waziri, baada ya Bunge hili kwisha niwaombe twende wote Jimbo la Mlimba mkaone utajiri wa Jimbo lile kwenye kilimo. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Fedha na Mipango
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. Nianze mchango wangu kwanza kwa kuipongeza Wizara ya Fedha katika eneo kubwa moja, Wizara ya Fedha sasa imeona umuhimu wa kupeleka walau fedha kwa kiwango kidogo kwenye sekta ya ardhi ili kusudi tuanze kufanya vizuri kwenye ardhi. Pia niipongeze Wizara ya Ardhi, wakati Mheshimiwa Waziri anawasilisha bajeti yake ya Wizara aliona umuhimu wa ushiriki wa sekta binafsi katika upangaji na upimaji wa nchi yetu. Kwenye eneo hilo nampongeza sana Waziri na Naibu Waziri na Wizara nzima ya Ardhi kwa ujumla.

Mheshimiwa Spika, naomba niongelee tu ardhi namna gani itatupa fedha, sigusi eneo lingine siku ya leo. Naomba nianze mfano wa Japan, Japan kabla hawajakwenda kwenye mapinduzi ya teknolojia waliwekeza kwenye ardhi pamoja na kuwa na ardhi ndogo, ukienda pake Tokyo idadi ya wakati wa Tokyo inakadiriwa kuwa takribani milioni 30, ni eneo dogo sana lakini ardhi ile ya Tokyo imepangwa vizuri na majengo yakajengwa kwenda juu. Walivyoona ardhi haitoshi wakaenda kwenye mapinduzi ya teknolojia, leo hii Japan ni nchi kati ya nchi saba zenye uchumi mkubwa duniani.

Mheshimiwa Spika, nirudi nchini hapa kwenye ardhi yetu, inakadiriwa watu waliomilikishwa viwanja, waliomilikishwa Tanzania ni watu 1,500,000 tu katika population ya watu milioni 60. Sasa nazungumzia tax base; watu 1,500,000 ndio wanaweza kulipa kodi ya ardhi lakini pia transactions ambazo zinatuletea fedha kwenye transfer kwa mfano wanauziana viwanja watu hawa hawa watu 1,500,000 hawa hawa tu nchi nzima katika idadi ya watu milioni 60. Tufanye hesabu ndogo tu, tukiweza kufikia lengo walau tupate watu milioni 10 tu Watanzania, tuache kwa sababu population karibu watu milioni 67, utaona kuna watoto, kuna wazee, kuna vijana ambao hawawezi kumiliki ardhi.

Mheshimiwa Spika, tuseme tu, tufikie uwezo wa kumilikisha watu milioni 10, leo hii nchi hii itakuwa na fedha kiasi gani? Milioni kumi tu, tusiende mbali zaidi. Kwa hiyo, niseme tu kwamba returns on investment ya ardhi ni ya muda mfupi sana kuliko uwekezaji wowote nchini. Hata mtu mmoja mmoja tu, wenye ardhi, wewe mwenyewe utaona tofauti ya mtu mwingine.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nasema neno moja hapa. Narejea tena, mfano nimetoka Japan narudia hapa Tanzania, Dodoma. Sizungumzii mambo makubwa sana, hapa hapa Dodoma. Natoa mfano halisi; wakati Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu inakwenda kuondolewa, walifanikiwa kupima viwanja takriban 69,000 kwa miaka yote 43, lakini Manispaa na Jiji baadaye ikapima viwanja 200,000; impact imeonekana ndani ya miaka mitatu. Niliwahi kusema hapa Bungeni, viwanja 200,000 vilivyopimwa na Jiji la Dodoma hatukwenda kukopa fedha benki, hatukupewa fedha ya Serikali Kuu. Sasa nimempongeza Waziri wa Ardhi kwa nini? Alivyokiri kwamba Serikali peke yake haiwezi ikapima ardhi ya nchi hii, nampongeza sana.

Mheshimiwa Spika, kwamba sasa sekta binafsi ikapime. Mfano, nafikiri Wizara ya TAMISEMI na Wizara ya Ardhi wanaweza wakakubaliana pamoja kwamba tuna Halmashauri 100 au takriban 84; Makampuni haya ya upimaji yakakabidhiwa hizi Halmashauri. Kuna maneno yalikuwa yakizungumzwa kwamba wale Makampuni ya Upimaji ni matapeli. Kuna sehemu tulikosea ndiyo maana wakapata nafasi ya kutapeli. Leo hii Mkurugenzi wa Halmashauri akienda akaingia mkataba na kampuni, Mkurugenzi wa Halmashauri, yeye ni answerable. Wananchi wao wanataka huduma tu.

Mheshimiwa Spika, hapo awali tulikuwa tunasema Kamati za Ardhi, ngazi ya mitaa ziingie mkataba. Haiwezekani, ndiyo maana tuliona imeshindikana mpaka wakaanza kutapeli wananchi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba na ni rai yangu, kwa dhati kabisa, model itakayotusaidia nchi hii kupata fedha nyingi ni ardhi. Tuache kote, tukiipima nchi yetu vizuri, kuna zile neighborhood zinazochangamka, Halmashauri za mijini mijini; ukienda pale na uzuri Waziri ameshatoa bei elekezi ya kulipia shilingi 150,000/=. Mwananchi wa kawaida akipimiwa kiwanja chake, shilingi 150,000 atalipa. Kwa sababu anaamini akipimiwa kiwanja ardhi yake inapanda thamani, atakopesheka, kama ni shamba atapata mkopo, atalima vizuri. Pia kama ni kiwanja, anaweza kukiuza kikawa na thamani ya juu zaidi, akawekeza kwenye maeneo mengine.

Mheshimiwa Spika, pia kwa faida ya Serikali; kiwanja kilichopimwa na chenye hati faida yake ya kwanza, Serikali inapata kodi ya ardhi ya kila mwaka. Sasa chukua kodi ya ardhi ya kila mwaka na hii ni kodi endelevu, huna haja ya kufanya mapitio tena. Kwa hiyo, ndani ya miaka yote wewe kodi ya ardhi unalipa tu. Kwa hiyo, niseme tu kwa dhati, ardhi ni sekta muhimu…

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

SPIKA: Ndiyo, taarifa Mheshimiwa Naibu Waziri Ardhi.

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napenda kumpa taarifa mzungumzaji ya kwamba nia njema ya Serikali kushirikisha taasisi binafsi katika upimaji, nadhani tumeiona. Tume-engage makampuni Zaidi ya 163, lakini matokeo yake katika utekelezaji wao, zaidi ya asilimia 60 kama haifiki 70 kati ya 60 na 70 wote wameshindwa kufanya kazi yao vizuri na Serikali iliwaamini.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, katika suala zima lile analolizungumzia, Serikali tayari ilishachukua hatua, lakini tunachohitaji sasa ni Halmashauri ambazo zinahusika kule kuweza kukaa na ile mikataba na wale watu kuweza kuwatambua badala ya kuwaachia wananchi. Ukiwaachi wananchi peke yake, zoezi haliendi. Kwa hiyo, tunahitaji commitment ya Halmashauri ambazo ndiyo Mamlaka za Upangaji, nasi ni Waheshimiwa Madiwani. Nadhani tukiweza kulisimamia kasi ya upimaji itaongezeka.

SPIKA: Mheshimiwa Kunambi unapokea taarifa?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ndiyo maana nimepongeza Wizara. Anachokisema Mheshimiwa Naibu Waziri ni cha msingi kabisa. Hapo mwanzo walipitisha Wizara ya Ardhi mwongozo unaosema, Kamati za Ardhi ngazi ya Vitongoji na Vijiji ndiyo viingie mikataba na ndiyo maana wananchi wakaanza kutapeliwa. Sasa Serikali imekwenda imepiga U-turn na ni jambo jema sana kwamba turudi sasa, kumbe tulikosea. Unaona!

Kwa hiyo, anachoeleza Naibu Waziri ni jambo la msingi kabisa kwamba sasa Halmashauri ndiyo ziingie mikataba kwa kupitia Wakurugenzi na siyo Kamati za Ardhi ngazi ya Vijiji au Mitaa. Huko tulikosea. Kwa hiyo, model hii mpya waliyokuja nayo, ndiyo maana nimepongeza Wizara ya Ardhi, ni nzuri kabisa kwa maslahi mapana ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka kusema nini hapa? Ninachoomba, Wizara ya Fedha iiongeze fedha Wizara ya Ardhi ili kusudi sasa kazi ya Wizara ya Ardhi isimamie upatikanaji wa hati kwa wakati. Kuna mfumo mmoja unaitwa ILMS (Integrated Land Management System). Mfumo huu ni mzuri sana. Tuliwahi kupata ufadhili tukapeleka pale Kinondoni, Kigamboni na Dar es Salaam kwa ujumla, umefanya vizuri. Leo hii nampongeza pia Waziri wa Ardhi, wameuleta hapa Dodoma.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu uzuri wake, Afisa Ardhi mmoja anaweza kutengeneza hati 300 kwa siku moja tu. Leo hii Afisa Ardhi mmoja anaweza kutengeneza hati tatu kwa siku, tena huyo ni mwadilifu sana. Kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri, tupeleke fedha Wizara ya Ardhi waka- integrate huu mfumo nchi nzima. Kila Halmashauri, wakati sekta binafsi inakwenda kupima, viwanja vinapatikana, basi wananchi wapate uhakika wa kupata hati. Kwa hiyo, maana yake nini? Mfumo huu ukiwa kwenye kila Halmashauri nchini, maana yake hati itapatikana kwa wakati; na kwa sababu tunataka tupate hati, na Land Rent itapatikana na tozo ya ardhi itapatikana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ninachokiomba kwa Waziri wa Fedha, kuna shilingi bilioni 50 nimesikia inaenda huko. Kwa hiyo, waone namna ya kuboresha boresha huko ili kusudi Wizara ya Ardhi isiishie Dodoma tu kuleta huo mfumo wa ILMS (integrate Land Management System), upelekwe nchi nzima ili kusudi Watanzania tupate hati na tulipe kodi na hii ni tax base kubwa.

Mheshimiwa Spika, nasema mathalan, tukipata watu milioni 10 tu wanaweza kukulipa kodi ya ardhi kwa mwaka, sisi bajeti yetu inakwenda ku-double na transaction za ardhi ni nyingi. Kwenye transfer tu kuna 10% ya bei ya kiwanja. Ten percent ya shilingi milioni 60 ni shilingi ngapi jamani? Hela iko huko. Nami sitachoka kusema, nitasema mpaka namaliza Bunge langu, mpaka nione Serikali imesikia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, suala la ardhi ni ardhi-mtaji kwetu Watanzania. Nitaendelea kusema mpaka nione Serikali imenisikia ili tupate fedha tukajenge madaraja, tupate fedha tumalizie miradi mikubwa ya kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema, nakushukuru sana, sana, sana. Naendelea kupongeza Wizara ya Fedha na Wizara ya Ardhi. Sisi Wabunge kazi yetu, naomba tuchukuliwe positive.

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ahsante sana.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante.
Hali ya Uchumi wa Taifa kwa Mwaka 2020 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 pamoja na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nikupongeze kwa kweli unatuwakilisha vema sisi vijana hapo kwenye kiti chako; hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Rais Mama yetu Samia Suluhu Hassan kwa bajeti hii nasema kwa dhati kabisa kuna msemo mmoja wa kingereza unasema all starts well ends well na katka hili niseme bila kuwa na kigugumizi ama kwa hakika legacy ya hayati Dkt. John Pombe Magufuli kamwe haitafutika kwenye ramani ya Tanzania. Kwanini haitafutika tunaye Mama yetu ambaye anakwenda kukamilisha kazi waliyoanza pamoja na hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na nimpongeze kwa ubunifu mkubwa Mheshimiwa Rais na kauli yake mbiu ambayo anasema kazi iendelee. Jambo hili la msingi kabisa na kupitia bajeti hii tunaona kwamba bajeti hii imetoa taswira na dira kwa Taifa letu, inakwenda kugusa wananchi wa hali ya kipato cha chini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lakini unapoongeza ushuru wa forodha kwa bidhaa zinazotoka nje ya nchi maana yake nini? Unalinda viwanda vya ndani lakini pia unaongeza unachagiza ujenzi wa viwanda ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, nampongeza Mheshimiwa Waziri kaka yangu Dkt. Lameck Mwigulu Nchemba kwa dhati kabisa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme kwa dhati hapa waingereza wanasema normally people they do not care how much know until they know how much you care! Maana yake nini siku zote watu huwa hawajali jinsi gani unajua mpaka waone jinsi gani unajali. Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mwigulu Nchemba katika hili wewe ni Daktari kweli kweli, siyo wale madaktari wengine wewe ni PHD holder wa kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu umetafsiri uchumi wa nchi yetu kwenye bajeti hii, hivi vitu siyo vya kawaida sana ndiyo maana vitu hivi lazima akili kubwa ifanye hivi kwa kweli nakupongeza na pamoja na Naibu Waziri kaka yangu Mheshimiwa Eng. Masauni mchape kazi sisi tuko nyuma yenu tutawaunga mkono. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa sababu kuu zifuatazo ya kwanza tunaona leo hii kulikuwa na ugumu wa makusanyo ya kodi ya property tax halmashauri tulipata shida kidogo huko nyuma, baadaye TRA nayo haikufanya vizuri. Lakini leo hii unapokwenda kukusanya kodi za majengo kwa kutumia bill za umeme kwa kweli tunakwenda kukusanya na naamini tunaenda kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na niseme kuna changamoto hapa mbili ambazo watu walikuwa wakizungumza wanasema kuna watu hatutumii umeme tunatumia solar power sijui kuna watu tunaweka umeme kabisa. Nishauri hapa katika watu wa kundi hili tuwaache halmashauri waendelee. Kada hii ya watu ambao wanatumia solar panel na watu wasiotumia umeme au hawajaunganishiwa umeme ile kodi iendelee kukusanywa na halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la mpangaji, sijui na mwenye nyumba hii hamna shida hapa ni jambo ambalo linawekwa kwenye mkataba tu na ni mahusiano kati ya mpangaji na mwenye nyumba na mlipaji na mwenye nyumba. Kwa hiyo, ni jambo ambalo yaani hatuitaji akili kubwa sana kwenye tafsiri hili kwa hiyo, nakupongeza sana kaka yangu Mheshimiwa Dkt. Mwigulu muendelee sisi tutaendelea kuwaunga mkono.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo jingine niendelee nijikite kwenye sekta nyingine ni sekta ya ujenzi. Tunapozungumzia sekta ya ujenzi ni sekta muhimu sana kwa ukuwaji wa uchumi wa Taifa letu kwa sababu moja kuu kwanza inakwenda kurahisisha huduma za usafirishaji wa bidhaa, bidhaa kutoka viwandani kwenda kwa watumia lakini bidhaa hasa za kilimo kutoka mashambani kwenda kwenye masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme tu ninashukuru sana na ninampongeza Waziri wa Fedha lakini pia nampongeza Waziri wa Wizara ya Ujenzi, unavyozungumzia miundombinu unazungumzia pia barabara kuna suala hapa kimsingi limegusa wananchi waJimbo la Mlimba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, itoshe tu kusema, Waheshimiwa Madiwani wa halmashauri ya Wilaya ya Mlimba wako kwenye ukumbi wa Spika na wanasikiliza na wenyewe wamekuja kupongeza Wizara hii muhimu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka kuzungumzia nini? Barabara hizi kuu tunaziita barabara za Mikoa zinaunganisha makao makuu ya mikoa na mikoa faida yake ni kubwa mno. Kwa sababu kwa mfano hii barabara inayokwenda kujengwa kutoka Ifakara Mlimba, Madeke, Lupembe mpaka pale Kibena Junction, barabara hii inaunganisha Mikoa miwili, Njombe na Morogoro faida yake ni nini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Mlimba ambao tunatoka Morogoro sisi tunalima Mpunga, lakini wananchi wa Njombe wenzetu wanashughulika na mazao ya mbao kwa hiyo, tutakwenda comparative advantage katika uchumi, maana yake wao wanatupa mbao tunanunua sisi tunawapa mchele wanakula. Kwa hiyo, ni neema kwa wananchi Mkoa wa Morogoro na neema kwa wananchi wa Mlimba lakini haitoshi hata Jirani zetu wa Njombe. (Makofi)

Mheshimiwa mwenyekiti, niende kwenye sekta ya ardhi, nikushukuru tena kwa mara nyingine Mheshimiwa Waziri, kitendo cha kupunguza kwenye marekebisho ya Sheria ya Sekta ya Ardhi tunaona Mheshimiwa Waziri unafanya marekeabisho ya Sheria ya Ardhi Sura Na.113 na unatueleza kwamba tozo ya mbele yaani premium inakwenda kupungua kutoka asilimia 2.5 mpaka asilimia 0.5 jambo hili ni la kheri kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka na naomba niseme kwa dhati, Serikali hii ni Serikali sikivu katika mchango wangu wa awali nilichangia kwa habari ya eneo hili, mheshimiwa Waziri umesikia na umekwenda kupunguza leo naomba nishauri jambo lingine bajeti ijayo muliangalie hili pia. Kuna hii kodi ambayo tunaita capital gain tax yaani kodi ya ongezeko la mtaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kodi hii inadumaza sana biashara katika sekta ya ardhi, kodi hii ya asilimia 10, Mheshimiwa Waziri bajeti ijayo nakushauri kaka Mheshimiwa Dkt. Mwigulu Lameck Nchemba, bajeti ijayo tupunguze kutoka asilimia 10 ije asilimia 5 itasaidia transaction za kuuziana kwenye sekta ya ardhi na ita-bust uchumi wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini eneo lingine naomba nishauri ni suala zima la upimaji hapa nimeona na nimeangalia takwimu hapa kwenye sekta ya ardhi mwaka wa fedha ukisoma kitabu cha Hali ya Uchumi wa Taifa ukurasa wa 203 inaeleza; Mwaka wa Fedha 2020 viwanja vilivyopimwa nchini na mashamba ni 337,970 kwa mwaka 2020 lakini kati ya hiyo viwanja 90,000 vinatoka Dodoma sawa na asilimia 40 ya upimaji kwa nchi nzima ni takwimu hizi zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndio maana nikasema sasa tunaona umuhimu wa sekta binafsi ku-engage kwenye shughuli za upimaji na upangaji wa nchi yetu. Dodoma tumefikia viwanja 90,000 kwa sababu tumetumia sekta binafsi na niseme tu nitaendelea kusema sitasita kwenye eneo hili. Kwa sababu ni mafanikio kwa Dodoma nchi nzima 300,000, Dodoma 90,000 asilimia 40, kazi imefanyika, hili jambo halihitaji fikra ya juu sana ni jambo la kawaida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kidogo niguse kwenye eneo la kilimo lakini nizungumzie sana suala la masoko. Mlimba sisi tunalima mpunga sisi hatuhitaji masoko Mlimba, sisi tunachohitaji Mlimba, tunahitaji kuchakata mpunga kuwa mchele. Tufanye packaging transport tuuze Japan tuuze nchi nyingine ili tupate fedha za kigeni. Hili litatusaidia wananchi wa Mlimba sisi hatuhitaji masoko tunahitaji processing, unavyozungumzia kuchakata mpunga ukawa mchele ukafanya packaging uka-brand tutauza ndani na nje ya nchi na namna hii tu tuweze kusema tutapata fedha za kigeni na tutakuwa na favorable balance of payment ndani ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie kusema, baada ya kuchangia haya kwa kweli, mnyonge mnyongeni haki yake mpeni na niombe kwa Waheshimiwa Wabunge, mama yetu Samia Suluhu Hassan ameanza vizuri anahitaji tumsaidie na kimsingi tumpe ushirikiano wa kutukuka. Hoja yangu ya msingi ambayo leo ninaacha swali kwa kila mmoja wetu, Je. Are we genuine? Swali langu. Mheshimiwa Rais kwa dhati kabisa anahitaji ushirikiano wetu na kumsaidia swali langu niliache hapa leo katika Bunge letu, are we genuine? Ahsante naomba kuwasilisha. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru wewe binafsi, lakini katika mambo ambayo Watanzania hawatamsahau Hayati Magufuli ni pamoja na mapinduzi makubwa ya fikra. Yapo mambo tunayosema yanaonekana kwa kuona, lakini jambo kubwa ni mapinduzi ya fikra za Watanzania. Ndio maana come rain come fire, kamwe hatuwezi kuwabadilisha Watanzania vile wanavyomwamini Hayati Dkt. Magufuli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nieleze kwa habari ya mapato. Tunapozungumzia utelekelezaji wa miradi ya maedeleo ni lazima tuangalie pia suala zima la mapato, suala la mapato ni jambo mtambuka na sio kazi peke yake ya Wizara ya Fedha na TRA. Naomba nieleze hapa ili tuone namna gani tunaweza kupata fedha kwa ajili ya miradi yetu ya maendeleo. Wengi tunasema barabara, maji, umeme, kama tutasimamia vizuri na kama tutakusanya vizuri mapato, kamwe hatufanikiwa; nazungumzia suala mtambuka maana yake nini.

Mheshimiwa Spika, Wizara za kisekta zina jukumu kubwa sana kufikiri tofauti kuongeza tax base ya Taifa. Ninavyozungumzia tax base nazungumzia wigo wa mapato ili tuondokane na mazoea ya vyanzo vilevile tulivyovizoea. Mathalani unavyoongeza tija kwenye sekta ya kilimo maana yake utaongeza tax base, unavyoongeza tija kwenye viwanda na biashara unaongeza tax base, unavyoongeza tija kwenye utalii utaongeza tax base na kwa kuwa nina nafasi ya kuchangia wakati tunachambua hizi Wizara moja baada ya nyingine nitaeleza kwa undani zaidi.

Mheshimiwa Spika, eneo linguine, jambo kubwa lingine kubwa ambalo Hayati Dkt. Magufuli ambalo amelifanya ndani ya Taifa letu ni kuhamisha kwa vitengo Makao Makuu ya Nchi kuhamia Dodoma. Labda tu Waheshimiwa Wabunge nieleze kwa ufupi ya harakati za kuhamishia Serikali Dodoma. Mnamo mwaka 1966 aliyekuwa mdogo wake Hayati baba wa Taifa, Joseph Nyerere alipeleka Muswada Bungeni wakati huo wa kuitangaza Dodoma kuwa Makao ya Nchi, lakini baadaye Mkutano Mkuu wa TANU mwaka 1973 uliamua rasmi sasa Makao Makuu ya Serikali yawe Dodoma. Lakini zipo jitihada zilizofanyika na hayati Baba wa Taifa, pamoja na kuanzisha Wizara ya Ustawishaji wa Makao Makuu mwaka 1973 ambayo Waziri wake wa kwanza alikuwa Adam Sappi Mkwawa, Retired Speaker wakati huo akisaidiwa na Sir George Kahama kama Director General wa CDA.

Mheshimiwa Spika, na walifanya kazi kubwa sana; unavyioiona Area C ya leo, unavyoiona Area D ya leo, unavyoioana Uzunguni ya leo, ni kazi ya Adam Sappi Mkwawa na Sir George Kahama wakiongoza Wizara ya Ustawishaji wa Makao Makuu ya Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, jambo hili limechukua muda, baadaye akaja mzee Samuel Sitta, hatimaye mama Anna Abdallah alihudumu kama Waziri na baadaye mchakato uliendelea kwa sabbau ya changamoto ya vita mwaka 1978/1979 ya Nduli Idd Amin, kidogo political will ya kuhamisha Serikali ilipungua kwasabbau uchumi wa nchi yetu ulipita katika kipindi kigumu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, amekuja kutimiza ndoto za Hayati Baba wa Taifa. Leo hii sisi wote Wabunge tuliomo humu ndani ni wadau wa Makao Makuu ya Nchi. Na yapo mambo makubwa yamefanywa na Serikali ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, Hayati sasa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii unavyoitazama Dodoma, angalia sekta ya barabara, sekta ya afya, miundombinu mbalimbali, unaiona Dodoma kwa kweli ni makao makuu kwelikweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini naomba nishauri jambo kwasababu Mheshimiwa Rais wetu mpendwa wa sasa wa Serikali ya Awamu ya Sita, mama yetu Samia Suluhu Hassan –na ndiyo maana kauli mbiu yake inasema kazi iendelee. Maana yake pale alipoishia Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli yeye sasa anaendeleza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa misingi hiyohiyo, leo hii kama siyo mashahidi hapa Waheshimiwa Wabunge, tumeanza kupata changamoto sasa hapa Dodoma za huduma mbalimbali, hasa huduma ya maji, ukienda umeme kidogo na maeneo mengine. Naomba nishaui Serikali; changamoto hii inaletwa na changamoto kubwa ya uratibu wa namna ya kujenga Makao Makuu ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, leo hii utaona watu wa RUWASA wana bajeti yao, watu wa TARURA wana bajetyi yao, Jiji la Dodoma lina bajeti yake. Kwa hiyo, taasisi zote hizi za Serikali kila mmoja anapanga kivyake. TANROADS naye ana mipango yake, hatuwezi kutoka, hatuwezi kusogea. Na ndiyo maana leo hii utaona huna wa kumuuliza.

Mheshimiwa Spika, sasa ushauri wnagu, changamoto hii ya uratibu wa makao makuu ya nchi, nishauri jambo ikiipendeza Serikali, kwa kuwa Mheshimiwa Rais wetu aliyepo sasa anaendeleza kazi iliyoachwa na Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, ushauri wangu; ni lazima tuwe na chombo cha uratibu kinachoweza kuzifanya taasisi hizi zote za Serikali zizungumze pamoja. Kazi ni ndogo sana, zizingumze pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, unapozungumzia suala la umeme, pamoja na uwepo wa Jiji la Dodoma, chombo hiki kitakutanisha taasisi zote hizi za Serikali hapa Dodoma, na kazi yake ni kuratibu. Sasa inategemea vile Serikai itakavyoona inafaaa.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano wenzetu Uganda. Ukienda Uganda wana chombo ambacho wanakiita Ministry for Kampala Capital City na Waziri wake wa sasa anaitwa Bi. Betty Amongi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ukienda Nairobi wenzetyu wana Nairobi Metropolitan Ministry ambayo Waziri wake wa sasa anaitwa Bw. Kamau, lengo kubwa hapa ni kufanya – na hakuna gharama, naomba nishauri Serikali – hakuna gharama ya uendeshaji wa chombo hiki, ni uratibu. Kinachoongezeka ni hawa watu kwenye chombo lakini bado taasisi zinaratibiwa kwa bajeti zao isipokuwa sasa chombo hiki kinafanya hizi taasisi zote zizungumze lugha moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kinyume cha hapo, wakati wangunikiwa Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma tuliweza kufanya yale tuliyoyafanya. Unajua, niseme tu mtakuja kuyaona haya baadaye. Tuliona mambo yanakwenda vizuri, siyo bure, utashi wa mtu katika utendaji wa Serikali hauwezi kuwa sustainable. Na ndiyo maana nashauri hili, tuwe na mfumo mzuri kwa ajili ya kuhakikisha kweli tunakwenda kujenga Makao Makuu ya Nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika,baada ya kusema hayo, naomba nimpe elimu kidogo dada yangu, Mheshimiwa Mbunge wa Nkasi, maana mtoto akichezea wembe muache umkate. Alivyokuwa anasema Serikali anasahau kwamba kuna sheria ya asilimia 4.4.2 iliyopitishwa hapa Bungeni. Unavyosema vijana wapewe asilimia kumi zote determinant…

Mheshimiwa Spika, kumradhi, determinant…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Ya pili tayari Mheshimiwa, nakushukuru sana.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Lakini kwa Habari…

SPIKA: Ahsante sana; dakika kumi ni chache.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, siyo mbaya naunga mkono hoja. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo ya Taifa Unaokusudiwa Kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii, lakini mchango wangu utajielekeza sana nianze kwenye eneo la actors wa Mpango wenyewe. Maana kupanga jambo moja, kutekeleza jambo la pili, mipango yetu ni mizuri sana na kila mwaka tumekuwa tukiwa na mipango mizuri ya namna hii. Lakini nijielekeze kwa actors wa Mpango huu yaani watekelezaji wa mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitaanza kwa namna ambavyo sekta ya Utumishi wa Umma inapimwa. Taasisi zetu za Serikali zinapimwa kwenye uwajibikaji. Ukisoma Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura Na. 298 imeeleza kuhusu namna gani Watumishi wa Umma wanapimwa yaani kuna OPRAS inaitwa Open Performance Review and Appraisal (OPRAS). Mimi nimehudumu na nilikuwa Mtumishi wa Umma kama Mkurugenzi wa Jiji kwa kipindi cha miaka minne na miezi kadhaa, hapa Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna jambo gumu sana kwenye kumpima Mtumishi Umma ni kwenye ujazaji wa OPRAS. OPRAS ni formula tu na kama utaratibu ambao tumeuzoea hizi business as usual. Kumpima Mtumishi wa Umma au Taasisi za Umma kwa kutumia OPRAS nadhani jambo hili limepitwa na wakati. Ukitazama eneo hili la OPRAS, ukitazama nchi zingine kwa mfano wenzetu Rwanda, Kenya na nchi zingine wanatumia Performance Contract kwenye kuwapima watumishi wake. Leo hii nikiuliza hapa bahati mbaya najaribu kuangalia Waziri wa Utawala Bora, Utumishi wa Umma sijamuona, nikiuliza hapa ni watumishi wangapi nchini wameshushwa vyeo kwa kupimwa performance yao, si tuna OPRAS yes! Mimi nimehudumu na nilivyokuwa Mkurugenzi wa Jiji ni mamlaka ya nidhamu lakini ni mwajiri pia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimepata uzoefu hapo kidogo ni ngumu sana kumpima Mtumishi wa Umma kwa kutumia OPRAS, ni formula tu! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu tunaona Mheshimiwa Rais, anapambana kweli kweli, usiku na mchana kwa ajili ya Taifa letu, lakini namna gani anasaidiwa kupima performance ya taasisi zake? OPRAS nadhani imepitwa na wakati, tuanze sasa na mfumo ambao wenzetu wanautumia duniani nimetoa mfano wa nchi mbili, nimesema Rwanda, leo hii Kagame anavyomteua Mkurugenzi wa Taasisi au kiongozi yeyote anakuja anampa malengo ya mwaka na anamwambia ndani ya mwaka ukishindwa kutimiza malengo haya uje na resignation letter, yaani uandike barua ya kuacha kazi mwenyewe au vinginevyo. Sasa sisi tunapima kwa kuangalia Vyombo vya Habari na sasa hivi tunakwenda kwenye Vyombo vya Habari, hapana huu utaratibu haufai.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumsaidie Mheshimiwa Rais kwa mfumo wa performance contract ndiyo mfumo unaotumika sasa duniani, ndiyo mfumo wa kisasa, kila mtu ataachia ngazi mwenyewe wala huna haja ya kuhangaika na mtu, anapewa malengo kwa sababu tuna mpango mkakati, anapewa malengo na unaainisha majukumu yake, asipotimiza analeta barua tu ya kuacha kazi mwenyewe kwa level yoyote ile. Sasa OPRAS weakness nyingine inagusa tu Watumishi wa Kada za chini, leo hii taasisi zetu kwenye ngazi za Wizara tunapimaje?

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKTI: Taarifa. Nakuruhusu uko ulipo aah! Mheshimiwa Tunza.

T A A R I F A

MHE. TUNZA I. MALAPO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemuelewa mzungumzaji nataka tu nimpe taarifa na wananchi wa Mlimba naye wampe Performance Contract ili akimaliza miaka yake mitano naye wamuone ame-perform vipi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Kicheko)

MWENYEKITI: Actually, Wabunge mnapimwa kwa performance contract, kabisa tofauti na wafanyakazi, hakuna OPRAS kwa wapiga kura. Ume-perform unachaguliwa tena, huja-perform wajumbe wale wanakupiga nje kabisa. Mheshimiwa endelea nimetunza muda wako. (Kicheko)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante naomba niendelee.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tuna Waraka mwingine ukiachana na Sheria hii Sura, 298. Mwaka 2018 kulikuwa na Waraka wa Serikali juu ya jambo hili ninalozungumza hapa, wala siyo jambo geni. Sasa hoja yangu sijui inaishia wapi na ninaomba baadae kwenye hitimisho tungepata maelezo kwamba ule waraka maana yake Waraka ni sehemu tu lakini tunaweza kuona na mimi ushauri wangu mwishoni, sasa tuitazame upya hii Sheria ya Utumishi wa Umma, Sura Na. 298 tuifanyie mapitio upya, badala ya OPRAS tuweke Performance Contract. (Makofi)

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Ruhusa!

T A A R I F A

MHE. ISSA J. MTEMVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimpe taarifa mzungumzaji kwenye eneo la OPRAS na utekelezaji wake sasa hivi tunaona mwaka 2017 Watumishi wengi waliondolewa kazini kwa kigezo cha OPRAS. Tena hapa, OPRAS imetumika vibaya sana, kuna tick tu ya kujaza kwamba nipo form four bila kuthibitisha cheti nimekileta au sijakileta lakini ukizingatia mwajiri ndiyo mwenye sifa zangu zote wakati ananiajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo OPRAS imeondoa Watumishi zaidi ya 4000 na wameshindwa kuwarudisha kazini. Hata hawajapeleka cheti chochote cha Form Four wala Form Six, OPRAS tu imesema form four wakati miaka 20 kafanyakazi akiwa darasa la saba.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nampa mzungumzaji taarifa hiyo.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, sipokei taarifa hiyo. OPRAS haihusiani kabisa inahusiana na performance, nazungumza performance. Brother nazungumzia performance.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unanielewa nazungumzia performance. Kuondoka kwa Watumishi wa Umma hakuhusiani kabisa na OPRAS, OPRAS inapima.

(Hapa baadhi ya Wabunge walizungumza bila kufuata utaratibu)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunambi unaongea na mimi endelea. (Kicheko)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba wananitoa kwenye mstari ngoja niendelee tu. Namsamehe kwa sababu mimi ni Chief wa Waluguru ninamsamee aendelee kwa sababu yeye ni mdogo wangu huyu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze katika sekta ya kilimo, nitoke huko niongelee sekta ya kilimo.

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, Taarifa! (Kicheko)

MWENYEKITI: Taarifa!

T A A R I F A

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nimpe taarifa mzungumzaji Mheshimiwa Kunambi kwamba hata katika promotion za Utumishi wa Umma ni lazima OPRAS itumike. OPRAS ile inavyotakiwa kujazwa ni kwamba yule supervisor anamjazia subordinate wake, utendaji kazi wake na kuona lakini tunafanyia maboresho kwamba sasa tutaijaza ile OPRAS kutokana na job description yako mwenyewe badala ya kuwa one fit all sasa hivi itakuwa Mhudumu atakuwa na job description yake ambayo ataijaza pale, ukija Injinia atakuwa job description yake na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tutaendelea kuitumia OPRAS katika kupima performance ya Watumishi wa Umma, ila tu kuna vitu ambavyo vitaongezewa na ndivyo tutavitumia hivyo vigezo hata katika kuangalia namna gani tunafanya promotion katika Utumishi wa Umma.

MWENYEKITI: Hoja ya Mheshimiwa Kunambi ni kwamba, kupima performance kwa job description ni msingi mbovu. Pima performance kwa kupima performance indicators. Ulitakiwa ufanye, tumekupa kazi tarehe fulani, ulitakiwa ufanye 1, 2, 3, 4, 5, …10 umeyafanya? Watu hawafanyi kazi! Ndiyo maana Kunambi alitandika makofi baadhi ya watu hapa Mjini.

Mhehimiwa Kunambi endelea. (Kicheko)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba nijielekeze kwenye kilimo. Sekta ya Kilimo wote ni mashahidi ni sekta muhimu sana kwa Taifa letu na mchango wake hata kipindi hiki cha Covid kilimo ndiyo sekta iliyoongoza. Asilimia 26.9 ya pato letu la Taifa, ukiangalia inafuatiwa na sekta ya ujenzi na maeneo mengine lakini kilimo ndiyo tunasema sekta muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi niombe tu, nimeona kwenye mpango tuna miradi takribani 21 ambayo imekamilika kwa mwaka uliopita kwa Bilioni 7.5. Umwagiliaji utatusaidia sana kuinua kilimo chetu Nchini, nadhani Serikali sasa iongeze bajeti kwenye umwagiliaji lakini haitoshi siyo tu kwenye umwagiliaji tuwe na Agro-Base Industries, viwanda vidogo vidogo vinavyo chakata mazao ya kilimo kuwa bidhaa, tuwekeze huko. Lakini pia tuongeze tafiti za masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii mimi ni mkulima wa mpunga, nina mpunga ndani sijauza gunia moja sasa ni shilingi laki moja, kutafuta hilo gunia moja ni zaidi kama 112,000. Sasa unauza laki moja si hasara hiyo? Nimefungia mpunga ndani! Kwa hiyo, Serikali ijielekeze kufanya tafiti ya masoko pia, tulime kwa umwagiliaji lakini pia ifanye tafiti za masoko. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nihitimishe kwenye jambo la barabara. Bahati nzuri barabara ya Morogoro – Njombe border ni barabara inayofungua uchumi wa nchi yetu na ni barabara ambayo inakwenda kutoa huduma Mikoa ya Nyanda za Juu Kusini. Lakini barabara hiyo kwenye taarifa ya mpango nikiwa naipitia imenishangaza kidogo labda Mheshimiwa Waziri aje atolee ufafanuzi jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti ya mwaka wa fedha tulionao sasa, imeelezwa kwenye bajeti barabara hii kipande cha kilometa 125 kitaanzwa ujenzi na tayari upembuzi yakinifu na usanifu wa mradi umekamilika. Sasa taarifa ninazopata kwenye mpango ni kilometa 220 zinakwenda kufanyiwa usanifu, zinatafutwa kandarasi za usanifu na upembuzi yakinifu wa mradi huo.

Mheshimiwa Spika, barabara hii umuhimu wake ni barabara mbadala wa Kitonga, mnaufahamu umuhimu wa barabara ya Kitonga, mizigo kwenda Zambia, mizigo kwenda South Africa, mizigo kwenda Malawi inapita Kitonga, Kitonga ikifunga na bahati fulani wakati wa masika Kitonga ilifunga tulikaa karibu mwezi mzima haipitiki ile barabara, walipata shida sana wafanyabiashara wetu. Mbadala wa barabara ya kitonga ni hii Morogoro – Njombe Border ni ya uchumi wa nchi yetu na ina-service Mikoa ifuatayo ya Njombe, Mkoa wa Ruvuma, Mkoa wa Mbeya na hadi Mkoa wa Rukwa. Ukipima umbali kutoka hapo Makambako uje uitafute Mikumi kuna zaidi ya kilometa 400, ukitumia barabara hii kutoka Makambako - Njombe kuja Mikumi kilometa karibu 300 na kitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa inanishangaza sana kuona kwenye mpango naelezwa habari ya kilometa 220 tafuta Mkandarasi na ADB ndiyo financier sawa! Hoja yangu ya msingi, hizi kilometa 125 ambazo upembuzi yakinifu na usanifu wa kina za mradi zimekamilika na bajeti inaeleza kilometa 50 zianze kujengwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba maelezo ya kina kwenye hili. Ahsante sana. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Hesabu za Serikali kuhusu Taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Hesabu zilizokaguliwa za Serikali Kuu, Mashirika ya Umma na Kaguzi za Ufanisi kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa kuhusu Hesabu za Serikali za Mitaa zilizokaguliwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021, na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kuhusu Uwekezaji wa Mitaji ya Umma kwa Mwaka wa Fedha ulioishia Tarehe 30 Juni, 2021
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nianze kwa kuungana na waliotangulia kuchangia kumshukuru Mheshimiwa Rais hasa kwa kazi kubwa anayofanya ya kutuletea miradi mingi kwenye majimbo yetu.

Mheshimiwa Spika, nianze kwa kujieleza kwenye chimbuko halisi, chimbuko lenyewe la Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Mamlaka ya Serikali za Mitaa chimbuko lake tutakumbuka wote wakati wa Ukoloni Serikali za Kikoloni zilianzisha mamlaka hizi na waliziita Local Authorities, lakini walizigawanya kwenye makundi takribani matatu na zinazotuhusu Waafrika waliziita Native Authorities.

Mheshimiwa Spika, hapa nchini Tanzania, Hayati Baba wa Taifa mwaka 1997 aliamua kuziondoa Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Baadaye miaka ya 1982 aliona umuhimu wa kurudisha Mamlaka za Serikali za Mitaa na zikatungwa sheria mbili za Bunge; Sheria za Serikali za Mitaa Mamlaka ya Wilaya (Sura Na. 287) na Sheria za Serikali za Mitaa Mamlaka ya Miji (Sura Na. 288).

Mheshimiwa Spika, hali kadhalika mwaka 1998 tukawa na Sera ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Dhana ilikuwa ni kutengeneza mazingira wezeshi kwa wananchi na ugatuaji wa mamlaka ulikuwa unakusudia kwamba wananchi washirikishwe moja kwa moja kupitia mamlaka zao pale kuanzia ngazi ya Kijiji, Kata halikadhalika mpaka ngazi ya Wilaya.

Mheshimiwa Spika, baada ya kupitia taarifa ya CAG ukurasa wa tisa, taarifa inaeleza kwa habari ya udhaifu katika uwekaji wa mitaji wa Mamlaka za Serikali za Mitaa. Taarifa nimeitolea mfano, Manispaa Jiji la Dar es Salaam wamewekeza hisa takribani 24,036,348 kwenye Benki ya DCB zenye thamani ya Shilingi bilioni 5.77, lakini taarifa inaendelea kusema kwamba Benki hii utendaji kazi wake hauridhishi. Sasa udhaifu huu chanzo ni nini? Naomba nianze hapo.

Mheshimiwa Spika, leo hii hakuna mwongozo, sheria hata kanuni inayoweza kutoa mwelekeo au kuelekeza halmashauri namna gani zinaweza kufanya uwekezaji. Tuanze hapo. Hatuna mwongozo, sheria, au kanuni inayoelekeza namna gani halmashauri zetu nchini zinaweza zikawekeza mitaji. Ameendelea mbele zaidi akatolea mfano Jiji la Dodoma kwamba hapo awali ndani ya Jiji la Dodoma; ukisoma ule ukurasa wa tisa kuna mfano bora, mzuri wa Jiji la Dodoma kwamba limejenga Hoteli ya nyota tano pale Mji wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, nianze hapo. Jiji la Dodoma sisi tilijiongeza tu wakati huo na nitangaze maslahi, nikiwa nahudumu kama Mkurugenzi wa Jiji la Dodoma. Nianze bajeti sasa, nitoe mifano ya namna gani mlolongo wa namna gani mapato ya ndani yalikuwa yakikua mwaka hadi mwaka hadi mwaka. Mwaka 2015/2016 bajeti ya Jiji la Dodoma ya Manispaa ya Dodoma bilioni 4.5 na makusanyo yalikuwa bilioni 3.6. Mwaka wa Fedha 2016/2017, makisio yalikuwa bilioni 3.9 na makusanyo yalikuwa bilioni 4.8 wakati huo, tukatumia bilioni 1.8 kupeleka kwenye miradi ya maendeleo, hapo awali ilikuwa ni ngumu hata kujenga choo cha shule ya msingi kupitia mapato ya ndani, tulianzia hapo. Mwaka wa fedha 2017/2018, makisio yalikuwa bilioni 20 kutoka bilioni 3.9, tukakisia bilioni 20 na tukafanikiwa kukusanya bilioni 25, tuka break even. Kwa nini tulikisia bilioni 20 kutoka bilioni 4.8?

Mheshimiwa Spika, tulikisia hivyo kwa sababu, mtakumbuka mwaka 2017 Hayati Dkt. John Pombe Magufuli aliondoa iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji wa Makao Makuu (CDA) na yenyewe ilikuwa na bajeti yake. Sasa mwezi Disemba tukafanya mapitio ya bajeti, wao bajeti yao tukaingiza kama bilioni 13 ambayo inatokana na viwanja na ya kwetu ikawa bilioni saba ikawa bilioni 20, lakini viwanja vile havikuwepo, ilikuwa ni bajeti tu kama bajeti. Tukavipima, ndio vikapatikana na tukapata hiyo bilioni 13 na tuka-break even kwa bilioni 25. Halikadhalika sasa mamlaka ya upangaji ikawa jiji kwa maana ya manispaa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwaka wa fedha 2018/2019, tukakisia bilioni 67, kutoka makusanyo ya bilioni 25, tukakisia bilioni 67, tuka-break even, tukakusanya bilioni
71. Tukasema viwanja muda unavyokwenda maana yake itafika mahali soko litapungua na sisi karibu asilimia 70 ya mapato tunategemea viwanja na ndio ilikuwa fursa kwetu Dodoma. Badaye nitarejea namna gani halmashauri nyingine zinaweza kufanya hivyo kwa fursa ambazo zipo huko.

Mheshimiwa Spika, tukasema hapana, Dodoma ni Makao Makuu ya Nchi, sasa haya mapato ya bilioni 71 yatakuwa sustainable? Jibu likawa hapana, sustainability, yaani uendelevu wa mapato hayo utafika mahali utashuka kwa sababu chanzo cha ardhi kikipungua hatuwezi kufikia hayo malengo. Tukakaa na management team yetu tukakubaliana tutafute uwekezaji ndani ya Jiji la Dodoma. Tukaona fursa pekee Dodoma, watumishi wanahamia, watu mbalimbali wanahamia, tukasema tuanzishe hoteli. Tujenge hoteli na hii miradi ni ya kimkakati, lakini pia tujenge nyumba za kupangisha watumishi, tulikuwa tunafikiria hivyo ili hii fursa tuitumie kama Makao Makuu ya Nchi.

Mheshimiwa Spika, tukaanza na hoteli. Pale Mji wa Serikali ule mradi uliitwa Government City Complex na lengo lilikuwa ni kujenga miradi mbalimbali hadi shopping mall pale. Kwa phase one tumefanikiwa kujenga hoteli ya bilioni 18. Naomba niweke sawasawa hapo, phase one ni bilioni 18, ile hoteli inayoonekana pale Mji wa Serikali na ni hoteli yenye hadhi ya nyota tano. Kama haitoshi tukatumia tena bilioni tisa kwa mapato ya ndani, sio mkopo wa benki wala fedha kutoka Serikali Kuu, tukajenga hoteli nyingine mkabala na White House, ukumbi wa pale Makao Makuu ya Chama Cha Mapinduzi ya bilioni tisa.

Mheshimiwa Spika, hii yote ilikuwa ni mikakati ya kuhakikisha kwamba, mapato yetu, demand ya viwanja ikipungua maana yake sasa hii inakwenda kuwa mbadala wake. Leo hii hoteli hizo nadhani wanatafuta operators ili zianze kuleta fedha.

Mheshimiwa Spika, nataka kusema nini? Ni kweli kuna udhaifu mkubwa kwenye namna ya miradi inayoanzishwa kwenye halmashauri, kwa nini? Hoja ileile, hatuna sheria, mwongozo wala kanuni inayoelekeza namna gani halmashauri zinaweza kuwekeza au kufanya uwekezaji. Niseme tu dhana hii ya sera yenyewe huko duniani, nitoe mfano mathalani Jiji la Pretoria, South Africa; ukienda pale Tshwane Metropolitan City Council wale wana-deal hadi na kampuni, wana idadi ya kampuni zaidi ya sita, wanatoa dividends to central Government, Tshwane Metropolitan City Council.

Mheshimiwa Spika, sasa huko nchi nyingine, ukienda vilevile Nigeria, majiji mengi duniani yanajitegemea yenyewe bila kutegemea Serikali Kuu. Sasa nchini kwetu ni tofauti kidogo, mathalani Jiji la Dar-es-Salaam. Nilikuwa naangalia hapa Jiji la Dar-es-Salaam, lenyewe kwa mwaka wa fedha 2021/2022 limekusanya bilioni 75, lakini leo hii recurrent ya Serikali Kuu inapeleka, mishahara ya watumishi inalipa Serikali Kuu. Bilioni 75 wanakusanya, lakini hata kamradi tu, hata kujenga tu zahanati, Hospitali ya Wilaya bado tunasema central government.

Mheshimiwa Spika, nataka kueleza hapo kwa hiyo, namna gani naweza kusema, lakini halikadhalika Kinondoni 49 bilioni, Arusha 23 bilioni, Mwanza bilioni 17. Nikirudi kwa maana ya fursa za halmashauri huko zilizoko, natoa mfano kule niliko kwa sasa Jimbo la Mlimba. Sisi bajeti yetu kwa mwaka ni bilioni 3.7. Tumetengeneza mpango wa kujenga kila mwaka kituo cha afya kimoja na mpaka sasa ninavyozungumza tunajenga vituo vya afya vitatu, Serikali kuu imetupa kimoja tu. Tunajenga Kituo cha Afya Chita, OPD imekamilika na tumefungua, Kituo cha Afya Kata ya Igima kinajengwa, lakini na vilevile Kituo cha Afya Kata ya Mofu kwa mapato ya ndani, 1.5 billion.

Mheshimiwa Spika, sasa kama Halmashauri ya Mlimba ndogo, yenye bajeti ya 3.7 billion inajenga vituo vya afya, hivi kweli na Dar-es-Salaam wanapiga magoti Serikali kuu? Majiji? Arusha Jiji? Ndio maana sasa matumizi mabaya ya fedha yanatokea kwa sababu, pesa haina matumizi. Wizara ijipange kutengeneza mpango kwenye majiji haya. Niliwahi kushauri huko nyuma watengeneze clusters kwa majiji na manispaa na ruzuku inavyokwenda waangalie, halikadhalika Wilaya. Kwa sababu, kwa mfano, nilikuwa naangalia pia halmashauri nyingine; kuna halmashauri zinakusanya chini ya bilioni moja, lakini fedha ya ruzuku ya maendeleo inaenda sawa na nyingine ambazo zinakusanya zaidi ya bilioni 10. Sasa Mheshimiwa Waziri kwa sababu yupo hapa hebu aliangalie hili ili tusiwe na uneven distribution of national income. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hatuwezi kupeleka fedha kwenye halmashauri zote ambazo zina uwezo wa kukusanya fedha kwa hiyo, lazima tuangalie, tutengeneze clusters. Cluster A, Cluster B, Cluster C, ili sasa tupeleke fedha za miradi ya maendeleo na recurrent kwa maana ya matumizi mengineyo ziende kulingana na mahitaji yao.

Mheshimiwa Spika, baada ya kumaliza hayo, niende eneo lingine. Mfano nilisema Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba, sisi tumekubaliana sasa, tumeanza, tumeshalima shamba la miti lenye ekari takribani 1,386, fursa tumeona ni miti. Nilivyokuwa Dodoma niliona hoteli ni fursa, kule tumeona fursa ni miti ya mbao, halmashauri zote zinaweza kufanya haya, Mungu alivyoiumba Tanzania ina fursa za kila aina kwa sehemu yao. Halikadhalika kule Songea wanaweza kulima hata mahindi, huku Rukwa wanaweza kulima hata mahindi ambayo ni miezi minne mitano unavuna.

Mheshimiwa Spika, sasa tukiendelea kusubiri kodi za wananchi, kama haitoshi tunalima pia na korosho na tumepanda ekari takribani 135 mpaka sasa. Nilikuwa nimesema Mlimba baada ya five years, huko nyuma nilisema Dodoma kwa sababu ndio Makao Makuu ya Nchi, kule actually tumeanza from the scratch, inawezekana.

Mheshimiwa Spika, changamoto tuliyonayo, narudia kusema, ni mindset, fikra. Wakati mwingine unaweza ukazungumza hapa kuwa kama uko sayari nyingine kumbe uko sayari hii hii.

Mheshimiwa Spika, changamoto ni fikra (mindset), utayari wa kuamua kufanya jambo (commitment), lakini mwisho uzalendo. Unakuta Mkurugenzi wa Halmashauri tangu ameteuliwa hata kubadilisha kiti hawezi, hata kiti tu. Hata kubadilisha mkao wa kiti tu. (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, kule South Africa nafasi hizi nyeti zinatangazwa watu wanaomba na wanamwita Municipal Manager, hawaiti Director, wanaita Municipal Manager, City Manager, wanatangaza kazi na watu wanaomba Professionals, sasa sisi mfumo wetu ni wa uteuzi. Sasa mimi najaribu kueleza hali halisi.

Mheshimiwa Spika, nijielekeze eneo lingine ambalo ni muhimu sana, eneo la Ofisi ya Mkaguzi wa Ndani Halmashauri. Ofisi hii ni muhimu sana, lakini tunaitazama kana kwamba, haina kazi, haisaidii chochote na ndio maana mianya ya wizi wa fedha ya Serikali unatokea. Leo hii uliza Halmashauri ngapi zina Mkaguzi wa Ndani ana gari? Anakaguaje miradi ya maendeleo wakati hana gari wala facility yoyote? Kwa hiyo nadhani Mheshimiwa Waziri aliangalie hilo. Lazima Ofisi za Mkaguzi wa Ndani ziwezeshwe zifanye kazi zao vizuri. Huyu ndio watch dog wa kwanza kwenye level ya halmashauri kule.

Mheshimiwa Spika, mwisho, nijielekeze kwenye eneo hili la Mfuko wa Mikopo kwa Vikundi. Tuna sheria nzuri kabisa na niwaambie fedha hizi zinazokwenda kwenye vikundi zina tija sana kwa wananchi wetu na sisi Mlimba, nataka nitoe mfano Mlimba, nataka kusema kwa sababu tunayafanya hayo; Mlimba sisi kila mwaka hatudai chochote, wananchi wanarejesha fedha zote, tumefanyaje? Naomba ku-share experience.

Mheshimiwa Spika, tumetengeneza utaratibu wa kugawana majukumu, kwa hiyo, Madiwani wao kwenye vikundi vya kata fulani anasimamia kurejesha fedha. Kama kata hiyo kuna kikundi chochote hakijarudisha fedha mikopo ijayo hakipati, kata hiyo haipewi kwenye mgawo. Kwa hiyo, inakuwa ni jukumu la Diwani kuwa mlezi wa kikundi na kuhakikisha fedha inarejeshwa kwa wakati.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo kwa kuwa kengele imelia, naomba kusema tu kwamba, nahitimisha mchango wangu hapo, lakini nakushukuru sana. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo wa Taifa kwa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026) na Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Mwaka 2021/2022 pamoja na Mapendekezo ya Muongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka 2021/2022
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, kwanza nimshukuru Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema aliyenijalia afya njema hata siku ya leo ikampendeza niwepo hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nimshukuru Mheshimiwa Rais lakini eneo kubwa nimpongeze, kwa kiwango kikubwa sana amefanya uwekezaji kwenye mtaji kama taifa. Mheshimiwa Rais anavyoelekeza jitihada kubwa katika ujenzi wa reli ya SGR anafanya capital investment (uwekezaji wa mtaji), anavyoimarisha bandari anafanya capital investment, anavyonunua ndege pamoja na jitihada za ujenzi wa Bwawa la Umeme la Nyerere anafanya uwekezaji katika mtaji. Maana yake nini? Maana yake Mheshimiwa Rais anatuandalia taifa ambalo miaka hamsini ijayo sisi akina Kunambi vijana wa leo na vijana wa kesho tutanufaika na mtaji huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme tu kwamba nimesoma mapendekezo ya Mpango wa Tatu wa Maendeleo ya Taifa wa Miaka Mitano. Nianze kwa kusema mpango ni zao la malengo, unavyotengeneza mpango lazima uanze na lengo ambalo litakupa mpango, mpango utakupa mkakati, mkakati unakupa mbinu, mbinu zinakupa mafanikio. Unavyokuwa na mpango lazima ujiandae na mikakati na mbinu za kutekeleza mpango ili tuweze kufanikiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite kidogo kwenye sekta ya kilimo na kaka yangu Mheshimiwa Bashe ni msikivu sana na naomba katika eneo hili anisaidie kidogo. Ukisoma ukurasa wa 88 mpaka 89 unaeleza habari ya sekta ya kilimo. Sote tunafahamu asilimia 65 ya Watanzania tunapata kipato kutokana na kilimo. Kama hiyo haitoshi kilimo kinachangia takribani 27% kwenye pato la Taifa na kati ya asilimia 27, asilimia 24 ni mauzo ya nje ya nchi na haya yameelezwa kwenye mpango huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado tuna kazi kubwa kwenye sekta ya kilimo, lazima tukubali. Kilimo chetu tunafanya subsistence agriculture, ni kilimo kwa ajili ya kula, not for surplus is for consumption kitu ambacho bado tuna safari ndefu sana. Nchi kama Tanzania yenye ardhi kubwa yenye rutuba lakini bado hatujaitumia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilipata fursa ya kwenda training ya quality structure system ya mwezi mmoja nchini Japan, nilishangaa sana. Nilikutana na Vice President wa JICA alinieleza maneno haya kwamba Japan kwa mwaka mzima wananunua chakula kutoka nje ya nchi ikiwemo Afrika lakini aliitaja Zimbabwe, why not Tanzania? Kama kuna nchi imebarikiwa ukiondoa Kongo inafuata South Africa na Tanzania ni nchi ya tatu kwenye rasilimali za nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, itoshe kusema pamoja na kwamba tuna changamoto ya funding kwenye sekta ya kilimo, lakini tatizo siyo funding inawezekana tukafanya mageuzi makubwa sana kwa kumuunga mkono Mheshimiwa Rais. Changamoto kwa Watanzania kuu ni tatu na siyo tu kwa level fulani, Watanzania wote tuna changamoto kuu tatu. Ya kwanza ni mindset. Marcus Garvey alisema neno moja, ukiwaza juu ya jambo lolote umeshindwa. Ukianza kwa kuwaza tu, mmh, nitaweza kweli umeanza kushindwa mapema na hutashida. Ni mindset kwa maana ya positive thinking. Ndiyo challenge tuliyonayo kwamba inawezekana, yes it can be done, kwa Mtanzania hiyo ni changamoto, unaanza kuwa na hofu kabla hujaanza safari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ya pili ni uzalendo, tulio wengi hatuipendi nchi yetu. Ndiyo maana utaona hata kwenye Utumishi wa Umma watu hawawajibiki. Ile OPRAS ningetamani iende kwa nafasi zote hata kwenye teuzi za Mheshimiwa Rais, kila mtu awe na OPRAS. Kama mtu anateuliwa apewe miezi sita hamna matokeo aondolewe tu. Unakuta kama ni Mkurugenzi, Mkuu wa Wilaya, Mkuu wa Mkoa anafika anakuta kiti kilekile na analazimika kukaa kiti kilekile mpaka anaondoka hata kubadilisha kiti hawezi, hata kubadilisha mkao wa kiti hawezi, wengi tuna changamoto hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni commitment, utayari juu ya jambo fulani. Itoshe kusema I am not speaking from without, I am speaking from within, nazungumza mambo ambayo nayafahamu. Naomba niseme hapa bayana lengo ni kujenga nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta ya kilimo kwenye suala zima la umwangiliaji bado tuna changamoto.

MWENYEKITI: Bado la tatu, umetutajia mawili.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, la tatu ni commitment (utayari). Tuna changamoto ya uzalendo, pili mindset kwa maana fikra chanya, tatu ni commitment, haya mambo matatu ndiyo changamoto ya Mtanzania siyo fedha, hatuna shida ya fedha hii nchi ni tajiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya kilimo tunatakiwa kufanya mageuzi makubwa sana. Kaka yangu Mheshimiwa Bashe pale Mlimba, Kata yangu ya Mgeta ina shamba ya hekta 5,000 mpaka leo zimetekelezwa. Serikali imewekeza kuna miundombinu ya umwangiliaji ndani ya hekta 3,000 na hekta 2,000 ndiyo bado na huu mradi hadi Baba wa Taifa miaka ya 1985 alipewa msaada na Serikali ya Korea lengo ni kuifanya Tanzania ipate uwezo wa kujikimu kwenye chakula. Ule mradi wamekwenda wajanja wajanja fulani mpaka leo umetelekezwa, Serikali imewekeza hekta 3,000 zina miundombinu ya maji ya kumwangilia hekta 2,000 ndiyo bado, hiyo ni fedha ipo pale, tungeenda kule tungefanikiwa. Kaka yangu Mheshimiwa Bashe naomba nimpeleke pale Mgeta, Jimbo la Mlimba akaone jinsi gani Serikali inapata hasara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni sekta ya ardhi, tuna changamoto ya kodi lakini ardhi ya Tanzania inaweza kutupa fedha nyingi sana. Bado sekta ya ardhi haijafanya kazi. Naomba niseme bayana na Mheshimiwa Waziri au Naibu Waziri naomba mnisikilize. Nchi hii inaweza kupimwa, tuna halmashauri 185 lakini leo hii Wizara ya Ardhi hata kupima halmashauri 50 hatuwezi, kuna haja ya kuendelea kuwepo hapo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nina mfano bora, Dodoma hii tunayoona leo, ndiyo maana nimesema naeleza nachokifahamu, Dodoma hii miaka mitatu iliyopita ilikuwa haijapimwa. Mimi ni mfano, Jiji la Dodoma tumepima viwanja 2,000 bila kupata fedha benki wala ya Serikali Kuu. Tukipima nchi hii kwenye halmashauri zote kazi ndogo sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaeleze jinsi gani wanaweza kupima nchi nzima, Naibu Waziri ananisikiliza. Umesajili kampuni za vijana wa Kitanzania ambao wamesoma, wakajiajiri, ukizipeleka zile kampuni zaidi ya 180, unazo Mheshimiwa Naibu Waziri kwenye ofisi yako, zikapime kwenye halmashauri zote, ardhi ikipimwa ni mtaji tunaongeza wigo wa kodi. Nitasema kweli daima, kuna pesa tunaiacha kwenye ardhi. (Makofi)

MWENYEKITI: Ndiyo maana nchi jirani, si mnajua tuna jirani nchi moja tu, tunazo nchi nyingi lakini moja ndiyo jirani zaidi, yule pale Kaskazini, ndiyo maana bajeti yao ni twice comparing with ours kwa sababu ardhi ya Kenya all most yote imepimwa ukiacha lile jangwa. Kwa hiyo, wanalipia every year ardhi yetu haijapimwa, nakuunga mkono. (Makofi)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Anachoweza kufanya Mheshimiwa Waziri wa Ardhi ni jambo moja tu, kuna vijana waliosoma land management na amewasajili, anazo kampuni zaidi ya 180, leo hii ana- discourage kampuni zisipime nasikitika sana. Namshauri aruhusu kampuni za vijana hawa wakapime kwenye halmashauri zote nchini. Yeye kazi yake wale vijana wakipima ardhi ile mwananchi atapata hati miliki, atakopesheka, uchumi wake utakua, kama ni shamba atakopa mkopo benki atalima. Vilevile wigo wa kodi unaongezeka yaani tax base ya nchi inaongezeka. Hizi kodi tunazokusanya ni ndogo sana sekta ya ardhi peke yake inatupa utajiri wa nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalize kwa kusema, leo nimesema maneno haya Mheshimiwa Naibu Waziri ikimpendeza kuna ule mfumo wa ILMIS awekeze pale, atafuta fedha awekeza kwenye mfumo, hizi kampuni binafsi ziende kwenye halmashauri zikapime. Waziri hana haja ya kupeleka fedha pale, hakuna haja ya hela, nimepima Dodoma viwanja 2,000 bila hela ya Serikali Kuu na kila mtu amepata ardhi hapa Dodoma viwanja bure inawezekana.

WABUNGE FULANI: Tunanunua.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Ndiyo unanunua lakini nimepima Dodoma karibia asilimia zaidi ya 50, kama kuna mbishi asimame hapa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nihitimishe kwa kusema kama kweli tunataka kumsaidia Mheshimiwa Rais Wizara ya Ardhi ijitathimini. Kwa kiwango kikubwa tunataka nchi hii iwe tajiri. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
Azimio la Bunge la Kutambua na Kuenzi Mchango wa Rais wa Tano wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa Utumishi wake Uliotukuka Pamoja na Azimio la Bunge la Kumpongeza Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema, aliyenijalia afya njema hata siku ya leo nikawa hapa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nianze kwa kuunga mkono hoja zote mbili, kwa maana ya maazimio yote mawili; lakini pili nijielekeze kwenye azimio la kwanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, Hayati aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli sisi, ulimwengu wa kimwili tunaona ametangulia mbele za haki lakini bado yu hai. Bado yu hai kwasababu matendo yake, aliyotutendea watanzania yatadumu milele. Na watu wenye vitendo vya namna hii, wenzetu waingereza wanasema immortality ni mtu ambaye anaweza kuishi angali amekufa. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini kazi kubwa ambayo mimi naomba nilishauri Bunge letu Tukufu; amefanya mambo makubwa ndani ya nchi yetu lakini kukumbukwa kwake kutakuwa ni jambo la msingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, ukienda South Africa pale Johannesburg, utaona kuna mnara pale lakini pia kuna sanamu nzuri sana ya Mandela, wanapaita Mandela Square. Kwa kazi kubwa aliyoifanya kuhamisha Makao Makuu yetu ya Nchi kuja Dodoma. Hapa Dodoma kuna eneo tengwa la Serikali na lina haki miliki maeneo ya Chimwaga; na Chimwaga tunafahamu kihistoria. Zaidi ya heka 100 zimetengwa pale kwa ajili ya recreational park, eneo la mapumziko. Niombe kushauri Serikali, ingefaa tujenge monument pale ambayo wajukuu, watoto wetu na kizazi kijacho kitakuwa kikisema Magufuli ni nani? Wanakwenda pale, na hii itatusaidia kumjengea heshima kubwa aliyotutendea Watanzania. Eneo lipo, zaidi ya heka 100 na lina hati ya Serikali na ni mali ya Jiji la Dodoma, kwahiyo hakuna mashaka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini baada ya kuzungumza haya nijikite kwenye eneo hili la Rais tuliyenaye Mama yetu mpendwa Samia Suluhu Hassan. Waingereza wanasema, all starts well ends well, all starts well ends well, mama ameanza vizuri, ametuonesha Watanzania kwamba kazi anaiweza. Mfano mzuri leo hii tumeona jina hapa la Makamu wa Rais. Ukitazama unaona matarajio yetu Watanzania, kwamba sasa yale yote yalioachwa na Hayati Dkt. John Pombe Joseph Magufuli yatakamilika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa nini nasema haya. Ukiangalia makamu wa Rais yeye amekuwa Waziri wa Fedha, lakini haitoshi, ni bigwa na mbobezi wa kukusanya mapato ya nchi haitoshi pia kubana matumizi. Kwahiyo hii chemistry ya Mheshimiwa Rais, mama yetu Samia Suluhu Hassan na Mheshimiwa Makamu wa Rais ni sawa na oxygen; yaani hydrogen mbili ukijumlisha, wale wana kemia ukichukuwa, ukichukuwa hydrogen mbili ukijumlisha na oxygen moja unapata maji. Kwa hiyo chemical reaction hii hatuna mashaka nayo, lazima maji yatapatikana.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nisichukue muda mrefu, itoshe tu kusema kwamba aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli ametubadilishia fikra Watanzania. Kuna watu tulikuwa tunaamini bila rushwa huwezi kupata huduma ya afya, lakini leo hii Watanzania tunaamini utapata huduma ya afya bila rushwa. Kuna watu tulioamini hakuna uwajibikaji ndani ya Taifa hili, lakini leo hii tunaona Taifa letu uwajibikaji umekuwa wa kutukuka na utawala bora.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo nisiseme sana lakini itoshe tu kusema nionge mkono maazimio yote mawili. Ahsante sana.
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. GOWDIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru, pia, niipongeze Wizara kuanzia Waziri mwenyewe mwenye dhamana ya Wizara na Manaibu wake lakini pia na Chief Executive wa TANROADS mzee wetu Mfugale. Kwa kweli wanafanya kazi nzuri. Kwa Mkoa wangu wa Morogoro pale Meneja wa TANROADS Mkoa Mhandisi Ntije, Mheshimiwa Waziri ikikupendeza aendelee kubaki na sisi Wanamorogoro tunamuhitaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nimepongeza Wizara kwa lengo kuu moja kwa sababu nimeona ukiangalia bajeti ya Waziri aliyowasilisha imeelezwa tunakwenda kuanza ujenzi wa barabara sasa ya kiwango cha lami ya kilometa 50 kutoka Ifakara kwenda Mlimba – Kihansi. Tumetengewa kwenye bajeti bilioni 7. Ukifanya hesabu ya kawaida unaona kama kuna kilometa saba au nane hivi.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini itoshe kusema kilometa 50 kwa bilioni 7 kwa kweli Waziri hebu tafakari tuone namna gani tunaweza kufanya ili wananchi wa Mlimba waone wanakwenda kupata barabara hii kwa wakati.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nimeona kwenye hotuba yake tunakwenda kufanyiwa upembuzi yakinifu wa kilometa 220. Barabara hii inaitwa Morogoro – Njombe – Boda yenye urefu wa kilometa takriban 220, hilo ni jambo jema na sisi tunataka kusema tu kwamba wana Mlimba wamesikia hakika tunaipongeza Wizara hii.


Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ni kuhusu upembuzi wa yakinifu wa barabara hii ya kilometa 220 ya Kihansi – Mlimba – Taweta – Madeke. Tangazo la kutafuta mkandarasi mshauri lilifanyika miezi mitatu iliyopita. Kwa hiyo, unavyokuja kuhitimisha bajeti yako jieleze tu ni lini sasa kazi hii ya upembuzi yakinifu inakwenda kuanza.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine ni suala zima la reli yetu ya TAZARA, ni mdau wa reli ile kwa sababu inapita Jimboni kwangu. Inaunganisha Dar es Salaam mpaka kule kwako Mbeya. Tumekuwa na vituo vidogo vinaitwa Hot stations na wananchi wa Mlimba ni wadau wazuri kwa sababu ni biashara na wanakuwa wanasafiri na watu wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna hot station inaitwa Chisano hot station, mpaka leo walifunga. Mheshimiwa Waizri, unavyokuja kuhitimsha bajeti, tusaidie ni lini wananchi wangu wa Tisano kata ya Tisano wanakwenda kupata Hot station hii ili nisishike shilingi yako na nitakusudia kushika shilingi kwa sababu hot station ni jambo la kuamua tu na ni biashara.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe hot station zote kwenye reli hii ziboreshwe kwa sababu wananchi hawa wanaotumia reli hii ya TAZARA wakati wa mvua wananyeshewa na mvua kwa sababu wanakwenda wanasimama tu njiani wanasubiri treni. Lakini jua likiwaka, wanawakiwa na jua. Kwa hiyo, kwa sababu ni biashara, kujenga mahusiano mazuri na wadau hawa wa hii reli ya TAZARA ni muhimu sasa Wizara muelekeze TAZARA wajenge vituo hivi vidogo kuboresha mazingira walau nyakati za mvua waweze kujistiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nimalizie kwa kusema tutafakari kwa kina ni namna gani tumegawanya miundombinu ya barabara Kitaifa. Leo hii kuna wenzetu wengine wanajadili barabara za Kata na Kata lakini kuna Watanzania hawafahamu tunavyozungumzia tumejenga barabara za lami Watanzania hawaijui lugha hii. Kwa hiyo, naomba niishauri Serikali, hebu kipaumbele kianze kuunganisha mikoa yetu yote tumalize, twende kwenye wilaya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wale wenye barabara za kutosha mpeleke fedha za maintenance, sisi wengine tujengewe barabara kwa sababu wananchi wa Mlimba hii barabara ya Morogoro – Njombe – Boda ni barabara ambayo inaunganisha Mkoa wa Morogoro na Njombe. Nadhani ipewe kipaumbele cha kwanza halafu wengine wafuatie kwa sababu nchi ni moja, walipa kodi ni Watanzania wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii maeneo mengine sitaki kuyataja, kuna Mbunge mmoja alikuwa anzungumza hapa anajadili barabara kitongoji na kitongoji, jamani nchi hii ni ya kwetu sote! Nchi ya Watanzania wote, wale ambao wameshajengewa barabara wakarabatiwe zile zilizojengwa ndiyo zijengwe mpya, hatuwatendei haki Watanzania wengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wasiwasi wangu kule kwenye Wizara tuwatazame wale wataalam wetu. Nina wasiwasi wanatoka mikoa fulani. Kwa hiyo, wanavyoandaa bajeti wanaandaa kwa makusudi ya kuangalia kwao wanakotoka, hii sio sawa sawa. Mheshimiwa Waziri katika hili naomba mkatafakari kwa kina, mchunguze hata kuangalia ukabila kabila kidogo. Samahani sisemi ukabila…[Maneno Haya Siyo Sehemu ya Taarifa Rasmi za Bunge]

NAIBU SPIKA: Hayo ondoa sasa hivi. Ondoa tu sasa hivi.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: … sizungumzii hiyo, sisemi hiyo....

NAIBU SPIKA: Ah! Wewe yafute ili yasiwepo kwenye kumbukumbu rasmi za Bunge.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niiondoe hiyo. Ninachotaka kusema ni kwamba watafakari kwa kina katika uandaaji wa bajeti tunazingatia vigezo gani? Yamkini kuna mambo fulani ambayo sisi wengine tunaamini ah! Sitaki kuendelea kusema maana nitaharibu huu mchango wangu. Itoshe tu kusema kwamba nashauri Serikali tujikite kwenye vipaumbele hasa barabara zinazounganisha mikoa na mikoa, twende kwenye wilaya. Tumalize kwanza hizi! Mkoa wa Morogoro unaunganishwa na Mkoa wa Njombe, Mkoa wa Morogoro unaungana na Mkoa wa Songea. Tukamilishe kwanza barabara hizi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Ofisi ya Waziri Mkuu
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nianze kuungana na Waheshimiwa Wabunge waliotangulia kumpongeza na kumshukuru Mheshimiwa Rais hasa kwa kazi kubwa anayoifanya katika kutuletea maendeleo Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya wananchi wa Mlimba tunamshukuru Mheshimiwa Rais kwa mambo yafuatayo: -

Mheshimiwa Spika, Halmashauri ya Mlimba ilikuwa haina hospitali ya wilaya lakini hadi sasa ninapozungumza hospitali ya wilaya inakamilika na tunatarajia mwezi Desemba huduma ianze kutolewa. Vile vile tunamshukuru Mheshimiwa Rais katika miradi ya maji. Tuna Miradi mikubwa ya Maji pale Mlimba Mjini inayokwenda kutoa huduma katika vijiji 11 ambapo Mradi wa Mlimba una thamani ya Shilingi Bilioni 3.7, lakini pia tuna Mradi wa Mbingu - Igima ambao thamani yake ni Shilingi Bilioni 3.6. Jambo hili jambo jema kwa wananchi wa Mlimba. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi, wakati naingia Bungeni hapa kwa mara ya kwanza nilieleza. Changamoto ya kwanza kwa wananchi wa Mlimba ukiwauliza ni barabara, changamoto ya pili kwa wananchi wa Mrimba ukiwauliza ni barabara na changamoto ya tatu kwa wananchi wa Mlimba ni barabara. Mheshimiwa Rais amesikia kilio cha wananchi wa Mlimba na kwa dhati kabisa namshukuru. Leo hii tunapozungumza Mheshimiwa Rais amekwishatoa kibali cha ujenzi wa barabara kwa kiwango cha lami inayoitwa Morogoro – Njombe Border yenye urefu wa kilomita takribani 222. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa awamu hii ya kwanza barabara hii itaanza kujengwa kilometa 100 kwa route mbili, route ya kwanza ni kutoka Ifakara mpaka Mbingu kilometa 67.5 na route ya pili ni kutoka Mbingu mpaka Chita pale Kambi ya Jeshi kilometa 37.5 na hiyo itahitimisha kilometa 100.

Mheshimiwa Spika, awamu ya pili kwa kilomita zilizobaki, Mheshimiwa Rais amepata kupitia mahusiano aliyojenga na Taifa letu na mataifa mengine hasa na taasisi za kifedha duniani. Benki ya Maendeleo ya Afrika imeridhia kufanya usanifu wa mradi wa barabara kipande kilichobaki cha kilomita 122 kutoka Kihansi mpaka pale Madeke, kwa maana ya upande wa Njombe. Katika hili tuna kila sababu ya kujivunia Mheshimiwa Rais na sisi Wanamlimba tunamwahidi ifikapo 2025 tutampa kura zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze kwenye eneo lingine, eneo la elimu na hasa leo hii nitazungumzia suala la elimu ya ufundi. Hapo nyuma elimu ya ufundi ilikuwa inatolea katika taasisi tatu. Taasisi ya kwanza ilikuwa Taasisi ya Sayansi na Teknolojia, tulikuwa na Vyuo kama Dar es Salaam Institute ot Science and Technology kwa maana ya (DIT), tulikuwa na taasisi pia ya Elimu ya Sayansi na Teknolojia kule Mbeya (Mbeya Institute of Science and Technology) na sasa hivi vyuo hivi viwili vyote vimepoteza hadhi hiyo. Leo hii ukienda Mbeya kuna Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia Mbeya sio Taasisi ya Elimu ya Sayansi na Taeknolojia. Ukienda Dar esSsalaam kuna Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Dar es Salaam na sio Taasisi ya Elimu ya Sayansi na Teknolojia.

Mheshimiwa Spika, vyuo hivi vimepoteza haiba ya kuzalisha wanafunzi ambao wanakuwa na maarifa na ujuzi na matokeo yake sasa Taifa letu tunakuwa na vyuo vikuu vingi na elimu ya chuo kikuu basically kwa asilimia kubwa inaandaa wanafunzi kwenda kuajiriwa. Hata hivyo, sio tu kuajiriwa inaandaa Managers, lakini elimu ya ufundi inaandaa watu wanaokwenda kuzalisha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, rai yangu, ombi langu na ushauri wangu kwa Serikali, ni muhimu sasa itazame upya suala hili na kwa sababu Taifa letu lina changamoto kubwa ya kada ya Mafundi Mchundo. Nieleze jambo hapa, katika safari yangu ya elimu nilibahatika kusoma Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi pale Kibaha, nilisoma elimu ya ufundi miaka miwili na nilisomea ufundi wa magari na mitambo.

Mheshimiwa Spika, vyuo hivi asili yake ni Sweden, Baba wa Taifa alianzisha vyuo hivi mahususi kulifanya Taifa letu liwe na vijana wengi wenye ujuzi lakini vyuo hivi leo hii vimesahaulika kabisa na nikisema nadhani hapa Waheshimiwa Wabunge watakuwa mashahidi, baadhi nikiwambia FDC ni neno jipya kwao leo. Kuna Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi ambavyo viko Kibaha, Ifakara pale kipo Chuo cha Maendeleo ya Wananchi Ifakara. Sasa vyuo hivi ni muhimu kwa sababu vinatoa ujuzi zaidi ya VETA. Vijana wanasoma elimu ya ujasiriamali, vijana wanasoma elimu ya uchumi na fedha, vijana wanasoma elimu ya uhasibu. Sasa ombi langu na ushauri wangu kwa Serikali ni muhimu sasa ikatazama vyuo hivi, fedha zipelekwe.

Mheshimiwa Spika, kama haitoshi, eneo la tatu la ufundi ni Vyuo vya VETA na hii namshukuru Mheshimiwa Rais, tumepata fedha Halmashauri ya Wilaya Mlimba kwa maana ya Wilaya ya Kilombero, tumepata fedha za ujenzi wa Chuo cha VETA na Chuo kile kinakwenda kujengwa pale Mlimba, Kata ya Mchombe, Kijiji cha Lukolongo. Kwa hiyo, hii ni fahari kwa wananchi wa Jimbo la Mlimba hususani wa Kata ya Mchombe na Kijiji cha Lukolongo. Tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ninapokwenda kuhitimisha hoja yangu, ni eneo la mahusiano baina ya Mamlaka za Upangaji na Wizara ya Ardhi kama Msimamizi wa Sekta ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika, hapo awali kwa mujibu wa Sheria Namba 8 ya Mwaka 2007 ya Mipango Miji, mamlaka za upangaji ni halmashauri zote nchini na mpaka sasa ipo hivyo. Changamoto inayojitokeza sasa kupitia Waraka wa Utumishi wa Ardhi, Watumishi wa Ardhi walihamishwa kutoka Halmashauri kwenda Wizara ya Ardhi, sasa nini nafasi ya Mkurugenzi wa Halmashauri katika kumsimamia Afisa Ardhi ambaye yuko kwenye Halmashauri yake? Kuna ombwe hapo, ndio maana leo hii migogoro ya ardhi imekithiri nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi yeye ndio mwajiri, yeye ndiye anayepandisha madaraja ya watumishi wa kada ya ardhi. Mkurugenzi wa Halmashauri anaambiwa na niseme kwa dhati, ukiangalia Maafisa Ardhi walioko kwenye halmashauri hawatofautiani na tunaita kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kuna mtu anaitwa Mshauri wa Mgambo, yule pale amekwenda kuhifadhiwa tu na wanashauriana na Mkuu wa Wilaya ila Mkuu wa Wilaya hana Mamlaka ya kumuagiza Mshauri wa Mgambo.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, leo hii nitoe mfano, Mkurugenzi wa Halmashauri amempangia kazi Afisa Ardhi, Kamishna wa Ardhi wa Mkoa naye anamwita, sasa huyu Afisa Ardhi anakwenda wapi? Anamsikiliza Mkurugenzi wa Halmashauri au anakwenda kwenye Mamlaka yake Mkoani?

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, Taarifa.

TAARIFA

SPIKA: Mheshimiwa Kunambi kuna taarifa kutoka kwa Mheshimiwa Angelina Mabula.

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii. Napenda nimpe taarifa msemaji asitake kupotosha. Waraka uliohamisha Watumishi wa Ardhi kwenda Wizarani ndio ule ule uliowataja watu wa TARURA, ndio uliotaja watu wa maji.

Mheshimiwa Spika, la pili, kiutendaji wale watu wako hundred percent kwenye halmashauri kwa sababu Halmashauri ndizo Mamlaka za Upangaji. Sasa hauwezi kuwa Mamlaka ya Upangaji usiwe na sauti na yule mtu. Kwa hiyo, kama analalamikia kwamba ardhi Mkurugenzi anakosa sauti, kwa nini TARURA wanafanya kazi? Kwa nini Wizara ya Maji wanafanya kazi na waraka uliohamisha majukumu ulikuwa ni ule ule mmoja? Wameletwa Wizarani kwa ajili ya ajira na nidhamu na adhabu zozote zinaanzia kwenye halmashauri husika kabla ya Katibu Mkuu kuweza kutoa. Kwa hiyo, hakuna ambacho kimeharibika katika hilo isipokuwa Wakurugenzi wanataka kukwepa majukumu yao kwa kusingizia kwamba hawa watu huwa wako Wizarani.

SPIKA: Mheshimiwa Kunambi unapokea taarifa hiyo?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, namheshimu sana Mama yangu, lakini sipokei taarifa hiyo. Labda nieleze, ukizungumzia TARURA ni independent, wanajitegemea hawako kwenye Halmashauri, ndio maana wanafanya vizuri, ukizungumzia watu wa Maji RUWASA ni taasisi inayojitegemea, hawako kwenye Halmashauri, sasa ukitoa Mfano wa RUWASA na TARURA hapana.

SPIKA: Dakika moja malizia.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, naomba nishauri, ili kuboresha ufanisi wa Sekta ya Ardhi nchini, Wizara ya Ardhi ikae na Wizara ya TAMISEMI, warejee huu waraka waone ni namna gani Mkurugenzi wa Halmashauri anakwenda kuwa na mamlaka ya kumwagiza Afisa Ardhi na watu wa mipango miji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Wakati najiandaa asubuhi ya leo kuja kuchangia Wizara hii wezeshi kwa sekta zote za uzalishaji nchini, nilimwomba Roho Mtakatifu anipe hekima, maarifa na busara ili niweze kuwatendea haki Watanzania wote wa nchi hii siku ya leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekuja na Ilani ya Chama cha Mapinduzi ya 2020/2025, nimekuja na hotuba ya Mheshimiwa Rais wakati anahutubia Bunge. Wakati najianda kuchangia, labda nieleze maeneo nitakayopita, eneo la kwanza ni kuhusu mradi, matumizi ya fedha za mradi wa bilioni 345 ambazo ni mkopo wa Benki ya Dunia, mkopo ambao kila Mtanzania atalipa, mimi nitalipa, wananchi wa Mlimba watalipa na wananchi wa Mlimba wameniambia katika hili hapana, wengine mkikubalia sawa lakini wananchi wa Mlimba wamesema hapana! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni migogoro ya ardhi, eneo lingine ni usimamizi wa watumishi wa sekta ya ardhi na mwisho nitahubiri kidogo injili. Nianze na mradi wa bilioni 345 mkopo kutoka Benki ya Dunia. Nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kulihangaikia Taifa letu kwa kutafuta fursa mbalimbali huko Duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi inasikitisha matumizi yake. Tumeambiwa na Kamati hapa bilioni takribani 46.8 zinakwenda kwa ajili ya uratibu, uendeshaji na dharura, katika Taifa ambalo limepimwa kwa asilimia 25 tu, katika Taifa ambalo lina vijiji takribani 12,318, vilivyopimwa ni viijiji 2,868 tu. Katika Taifa ambalo vijiji ambavyo havina mpango wa matumizi bora ya ardhi ni takribani 9,541, katika Taifa ambalo wananchi wamekuwa wakifa kila siku, watu wanakufa kutokana na migogoro ya ardhi, inasikitisha! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme kwa dhati maana ukichangia hapa kuna minong’ono huku wanasema huyu anataka uwaziri, kama uwaziri unakuja kwa ajili ya kuchangia acha uje tu! Kama kwa style hii acha uje tu. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Mwenyekiti, I am not speaking out of nothing, I am speaking on something that I know, nazungumza jambo ambalo nalifahamu sekta ambayo naifahamu vizuri sana na nime–practice sibahatishi kwenye ardhi na nimeweka matokeo makubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nieleze katika fedha hizi matumizi yake vijiji 500 tu vinakwenda kupimwa na thamani ya kupima kijiji, gharama ya kupima kijiji kimoja ni milioni 12 mpaka Milioni 15, kwa hiyo kwa vijiji hivi vilivyotajwa 500 itatumika fedha bilioni 5.5 tu katika mpango wa fedha bilioni 345 are we serious? are genuine? ni kweli tunamsaidia Mheshimiwa Rais? ni kweli are genuine? au tunasema tu mdomoni mioyo yetu inakataa, hapana mi bado ni kijana mdogo nategemea kutumikia Taifa langu kwa miaka ijayo. Kwa hiyo no matter what will happening to me lakini leo tasema ukweli daima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeeleza hapa nilijaribu kufanya tafiti kidogo nikajiuliza maswali asubuhi…

MHE. SOUD MOHAMMED. JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunambi kuna taarifa.

TAARIFA

MHE. SOUD MOHAMMED. JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba tu kumpa taarifa Mheshimiwa Kunambi kwamba upimaji wa ardhi ni process, siyo kama labda ni upimaji wa ardhi utapima tu mara moja. Kwa hiyo nilikuwa naomba tu kumwambia kwamba upimaji huu ile miundombinu ambayo inakwenda kutengenezwa ina saidia kuweza…

MWENYEKITI: Waheshimiwa Wabunge, naomba tusikilizane.

MHE. SOUD MOHAMMED. JUMAH: Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba tu kumfahamisha Mheshimiwa Kunambi kwamba ile miundombinu kwamba ambayo itakwenda kutengenezwa katika mradi huu wa uwishaji usalama na rasilimali za ardhi ndiyo utakwenda kusaidia kuweza kuipima ardhi kwa haraka baada ya kwisha kuitaarisha ile miundombinu. Ahsante sana.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Godwin Kunambi unaipokea hiyo taarifa?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua unapoteza muda kwa mtu ambaye any way siipokei. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sina mzaha hapa! Nimefanya hesabu ndogo tu ya kujumlisha na kutoa ambayo kila Mtanzania anaweza kuifanya. Ukipima vijiji 2,000 katika mradi huu fedha hii ya mkopo ambayo kila Mtanzania analipa, vijiji 2,000 thamani yake ni bilioni 30 tu. Ukipeleka bilioni 30 tu, na mimi nakutaarifu Mheshimiwa Waziri nakuja kushika shilingi nataka kuona bilioni 30 inakwenda Tume ya Taifa ya Mipango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilijaribu kuangalia Ilani nimesema nimekuja na Ilani naomba niisome, naomba ninukuu Ilani ya Chama cha Mapinduzi Chama changu kwa ufupi Ibara ya 74 Ukarasa wa 120 mwenye Ilani arejee, naomba nisome Chama cha Mapinduzi kimeelekeza Serikali kwa miaka hii mitano kupanga na kupima vijiji takribani 4,131 na Wilaya 54.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika fedha hizi unaenda kupima vijiji 500 huu ni mwaka gani huu? Mwaka 2023 bado miaka hii miwili, kutoka 2021 mpaka sasa Wizara wamepima vijiji 618 tutafika lengo hili la Chama? Ndiyo maana nauliza are we serious? Are we genuine?

MBUNGE FULANI: No.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Hapa tunacheza na changamoto za Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikajiuliza kuhusu migogoro ya ardhi, nikauliza wenzetu wa jirani wa Uganda hivi kuna migogoro ya ardhi Uganda? Wakasema Hapana, nikauliza Rwanda kuna migogoro ya ardhi? Wakasema hapana. Nikauliza hapa Kenya kuna migogoro ya ardhi? Wakasema Hapana! Migogoro ya Ardhi ni matokeo ya kushindwa kwa sekta nchini, nataka nipigie mstari hapo, migogoro ya ardhi ni matokeo ya kufeli kwa sekta ya ardhi nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi naomba nijielekeze kuhusu wasimamizi wa sekta ya ardhi. Kama kuna eneo Wizara imekosea kuwachukua watumishi kutoka Halmashauri kuwapeleka wakawasimamie mfano, wanasema TARURA, wanasema RUWASA, RUWASA ni taasisi inayojitegemea ndiyo maana ina perform, TARURA ni taasisi inayojitegemea ndiyo maana ina- perform, sasa Wizara imechukua tu watumishi mi nadhani basi waanzishe taasisi na wenyewe basi ili wapime na kupanga, iwe mamlaka ya upangaji isiwe tena Halmashauri wanawaonea tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee…

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Taarifa ya pili dakika mbili, hamna zaidi ya hapo, Mheshimiwa Musukuma.

TAARIFA

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Utanisamehe sana rafiki yangu Kunambi maana Bunge hili tuko live calculation unazozipiga unalipotosha Bunge na Watanzania. Kwa hesabu unazozipiga hata tunatoka kwenye Halmashauri, tunaongoza Halmashauri zetu tunajua tunapima kwa style gani, kuna kupima kwa kudhulumu na kuna kupima kwa kulipa haki za watu. Sasa calculation unazolieleza Bunge hapa na bahati nzuri wewe ulikuwa Mkurugenzi hapa na mimi nimewekeza hapa nime-deal na wewe, nakufahamu na Wabunge wote wako hapa, kwa style ya wewe uliyoifanya hapa tukiruhusu hizo hesabu zako Waziri akazichukua hii Tanzania tutachinjana kwa ajili ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. (Makofi)

MWENYEKITI: Mheshimiwa Kunambi, unapokea hiyo taarifa?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa. Ninachosema ni kwamba kinachofanyika sasa unasema mamlaka ya nidhamu ni Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi, Mtumishi yuko Kakonko, mtumishi yuko Mlimba hivi utendaji kazi wake kule anajuaje? Anasema kuna Kamishna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamishna yuko ngazi ya Mkoa na niseme kuna mgomo Mheshimiwa Waziri kama hujui nakusaidia, kuna wale Watumishi mliyowashusha vyeo Wakuu wa Idara, mtu alikuwa na mshahara alikuwa na mshahara 3,400,000 leo hii anakuwa Afisa Ardhi wa kawaida, wamegoma kwenye Halmashauri huko. Ndiyo maana hilo nenda kafanye uchunguzi nakusaidia tu na uchukue tu positive mchango wangu, nakupa tu hiyo siri kuna mgomo unaoendelea, wale watumishi mliowashusha vyeo huko kwenye Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyewkiti naomba nihitimishe, nahitimisha kwa mahubiri. Ukisoma…

MWENYEKITI: Muda wako umeisha.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti naomba dakika moja tu.

MWENYEKITI: Nusu dakika.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Dakika mbili tatu. Mtume Paulo kwa Wakorintho aliwahi kusema habari hii kwa Wakorintho jamani tusikilizane kidogo “Nikiitazama Dunia ni ubatili mtupu” lakini ndugu zangu kizazi chetu ni cha nne, uhai wetu ni miaka 70 jamani tafuteni kwanza ufalme wa mbingu mengine mtazidishiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Quran tukufu inasema maneno haya; “Quburwa Twanii’h ninal manii” kuipenda nchi yako ni sehemu ya imani Watanzania tuwe wazalendo kwa Taifa letu. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante awali ya yote nimshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa Rehma aliyenijalia afya njema hadi siku ya leo nikafika kwenye mkutano wetu huu. Pili nimshukuru Mheshimiwa Rais wote ni mashuhuda hakika anaendelea kufanya kazi nzuri ya kuendelea kutuletea maendeleo Watanzania. Niipongeze Wizara kwa maana ya Waziri mwenye dhamana Naibu wake kaka yangu Wakili Msomo Ridhiwan Kikwete lakini pia na watendaji wote wa Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, siku ya leo kwa kweli tunaona kuna improvement kubwa kwenye Wizara hii. Kwa sababu hadi mwaka wa fedha uliopita, nilikuwa najaribu kuangalia takwimu, viwanja vilivyopimwa nchini vilikuwa takribani milioni sita, lakini leo hii tumeona hapa kwenye hotuba ya Waziri wa Ardhi sasa tunakwenda milioni saba, tunaona kuna improvement.

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda kwa historia tu nieleze, hapa nchi yetu ilianza kupimwa mwaka 1896 ndipo kiwanja cha kwanza kilipimwa hapa nchini, sasa ukiangalia muda hadi sasa tulipofikia unaona bado tunakazi kubwa ya kufanya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nirejee maneno ya Hayati Baba wa Taifa, alisema nchi yoyote ili iweze kupiga hatua ya maendeleo lazima iwe na siasa safi kwa maana ya utawala bora, lakini watu na mwisho ardhi. Ardhi ni hazina kubwa sana kwa Taifa letu, na kila kitu unachokitaja kipo kama sio chini basi juu ya ardhi. Tukizungumzia madini ardhi, mito ardhi, kwa hiyo ardhi imebeba uchumi wa nchi yetu. Baada ya kueleza haya naomba nifanye comparison hapa na wenzetu jirani wa Kenya; nijaribu kuoanisha takwimu za Kenya na nchi yetu, (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tarehe 24 Aprili, 2021 saa Nne usiku Waziri wa Ardhi wa Kenya akihojiwa na Television ya the citizen alieleza kwamba nchi ya Kenya mpaka sasa wana hati miliki milioni 11. Sasa najaribu kulinganisha Kenya na sisi nikirejea kwetu mpaka leo tunapozungumza kupitia hotuba ya Mheshimiwa Waziri tuna hatimiliki yaani wananchi waliomilikishwa ardhi ni Milioni 2.3 utaona wenzetu wapo mbali sana, lakini naona kuna jitihada. Nimeeleza, mwaka uliopita hatimiliki nchini zilikuwa 1,500,000 tu lakini leo tunazungumzia milioni 2,000,000, kuna improvement. Sasa ushauri wangu ninaokwenda kutoa ni kuongeza kasi ya upangaji, upimaji na umilikishaji wa ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kwenye sekta hii ya upimaji Wizara ya Ardhi kama custodian au kama ndiyo mamlaka ya usimamizi wa sekta ya ardhi nchini, ushauri wangu kwake ingeendelea kubaki hivyo inavyofanya kuratibu na kusimamia sekta ya ardhi, na mamlaka za upimaji kwa maana ya Halmashauri kwa mujibu wa Sheria ya Mipango Miji Namba 8 ya Mwaka 2007 mamlaka za upangaji ni halmashauri. Sasa hoja ninayokwenda kushauri hapa ni lazima sasa Wizara Ofisi ya Rais TAMISEMI na Ardhi waje pamoja wawe na mpango wa pamoja. Kwa sababu kule kwenye halmashauri, halmashauri ziko chini ya Wizara TAMISEMI lakini ardhi ipo Wizara ya Ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Wizara hizi zinatakiwa zifanye kazi pamoja. Kwa mfano ukienda kwenye level za mikoa wasimamizi wa sera na shughuli za Serikali kwenye level ya mkoa ni Wakuu wa Mikoa. Ni muhimu sasa wakashirikishwa, wawe na ownership ya upimaji ili wasimamie vizuri zaidi. Serikali peke yake haiwezi kufanikisha jambo hili, lazima kuwa na engagement ya private sekta. Kuna kampuni za upimaji, hapo awali kulikuwa na hoja ya kwamba kampuni za upimaji hizi zimekuwa zikiwadhulumu wananchi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nadhani Mheshimiwa Waziri atakuwa ni shahidi, tulikosea mahali. Hapo nyuma ilikuwa kampuni zilikuwa zinakwenda moja kwa moja kukutana na wananchi, kamati za ardhi zinaundwa katika level ya vijiji au mitaa, halafu wanaingia mkataba ambao kimsingi hakuna mashiko ya kisheria kwamba anaweza kuwa huyo mkandarasi akikataa kufanya kazi na akiwadhulumu anaweza kuwajibika mahali popote pale. Sasa hivi naona kuna mfumo mzuri sasa, na mimi nishauri eneo hilo. Kwamba Wakurugenzi wa Halmashauri ndio waingie mikataba sasa na hivi kampuni au kandarasi za upimaji, mwananchi yeye asubiri huduma tu. Hii itatusaidia kudhibiti wizi au dhuluma kwa wananchi wetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nieleze faida za upimaji, ardhi ikipimwa kwa Serikali lakini pia kwa wananchi. Mwananchi akipimiwa ardhi yake iwe shamba anapata hati anakwenda benki anakopesheka, na jitihada za Wizara ya Kilimo maana yake mwananchi mwenye shamba anaweza pia akakopesheka na akaendelea kulima na nadhani nchi ikaendelea vizuri. Lakini pia si tu mkulima, mwananchi wa kawaida anaweza kufanya biashara. Akiwa na hati miliki anakopesheka, ardhi inapanda thamani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tukiongeza kasi upande wa Serikali, kwenye ardhi kuna tozo mbalimbali. Kwa mfano, mathalani kwa Mkoa wa Dar es Salaam. Mkoa wa Dar es Salaam una idadi ya watu takribani milioni sita. Tuchukue tu, tufanye sampling watu 1,000,000 tuwape hatimiliki za Dar es Salaam, hiyo fedha kiasi gani? tukipata milioni moja tu wenye hati miliki kwa Mkoa wa Dar es Salaam watatusaidia kuwa na sustainability mapato kwenye tozo za adhi. Kwa mfano kuna land rent mtu analipa, akifanya transaction ya kuuza kiwanja au nyumba analipa capital gain tax analipa stamp duty; hivi fedha zote ni maduhuli ya Serikali. Kwa hiyo mimi niendelee kusema tu kwamba pamoja na pongezi zangu kwa Wizara ya Ardhi tuna kazi ya kufanya ili kuongeza kasi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la pili ni eneo la mfumo wa ILMIS. ILMIS (Integrated Land Management Information system) ni mfumo ambao una hifadhi taarifa za sekta ya ardhi; na huu mfumo umeleta matunda bora. Leo Mheshimiwa Waziri amezungumza hapa, tunaona mafanikio ya hati hizi za kwenye mtandao; mwananchi akipimiwa; kwa mfano tunazungumzia viwanja milioni saba na tunazungumzia umilikishaji millioni mbili, kuna gape kama milioni tano hawana hati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa tukiongeza kasi hapo kwa mfumo wa ILMIS. tuka-integrate nchi nzima; na nimuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa sababu yupo hapa, na ananisikia; tukiongeza fedha kwenye Wizara ya Ardhi tukawawezesha wakai-integrate mfumo huu wa ILMIS, nchi nzima, na mtanzania akawa na uhakika akipimiwa kiwanja atapata hati miliki tutakuwa mbali sana. Kwa hiyo tuwekeze nguvu hapo kama Serikali ili tuweze kufanikiwa eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende haraka haraka kwenye eneo lingine, eneo la sekta binafsi nimeeleza lakini niombe kitu kimoja; sekta binafsi bado ina hali ngumu tutafute namna bora ya kuiwezesha, hasa kampuni za upimaji; kama kwa ruzuku au njia yoyote bora ambayo tunaweza kupeleka fedha au mikopo nafuu ili mtu akopesheke. Hii kampuni ya kijana wa Kitanzania aliyesajili kampuni yake, amejiajiri na anaajiri watu wengine, akiwezeshwa, kwa maana ya kama si ruzuku basi apewe mkopo nafuu; anaweza akafanya vizuri zaidi na nchi yetu ikapimwa kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende eneo lingine la migogoro ya ardhi, kumradhi migogoro ya ardhi ni matokeo tu ya failure sekta, tukiri kabisa, wananchi wanakimbia sana kuwekeza wanakimbilia sana kwenye ardhi, sisi kama Serikali bado tupo nyuma. Kwa hiyo migogoro ya ardhi ni matokeo ya failure ya sekta ya ardhi, wala si chochote, kwa hiyo tukisimama ardhi hii tukai-manage vizuri, tukaipima nchi nzima hata migogoro ya ardhi itakwisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, na hapa nirejee eneo moja; nimpongeze Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan. Mheshimiwa Waziri ameeleza hapa kulikuwa na migogoro ya ardhi kwenye vijiji 975, Mheshimiwa Rais mwenye mapenzi mema na Watanzania amesema sasa katika vijiji hivi havifutwi vyote Watanzania, vijiji 920 anasema vikarasimishwe, jambo hili ni la kumpongeza Mheshimiwa Rais, katika hili tumpongeze Mheshimiwa Rais; na siasa zetu zingekuwa ngumu kidogo kama vingefutwa hivi vijiji. Kwa hiyo leo hii, nadhani hata wananchi wa Jimbo la Mlimba wananisikia; kuna changamoto moja tu ambayo nimuombe Mheshimiwa Waziri aifanyie kazi. Bado kuna maeneo pale Jimboni kwangu yanashida. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Kata ya Mofu Kijiji cha Ikwambi na Karenga, leo hii watu wa TAWA bado wanawasumbuwa. Kwa hiyo nadhani ni muhimu sasa, kwa kuwa Serikali inakwenda kurasimisha vijiji hivi wenzetu hawa wa maliasili wangetulia kidogo na wananchi watulie kidogo mpaka Serikali itimize wajibu wake kwenye eneo hilo. Sasa, utekelezaji bado. Kwa hiyo pending ya utekelezaji ni muhimu sasa watu wa TAWA lakini pia na wananchi wangu wa Ikwambi na maeneo hayo niliyoyataja watulie kusubiri utekelezaji wa Serikali kwa kuwa Mheshimiwa Rais mwenye mapenzi mema na Watanzania amesema virasimishwe. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuhitimisha. Kata nyingine ni Kata ya Mchombe Kijiji cha Mbasa Kitongoji cha Shamba la Saba, Utengule na Ipugasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo niunge mkono hoja na Mheshimiwa Waziri naona hii chemistry, aa’ bwana, Mungu awabariki tu. Huko tunakokwenda naona tunakwenda kulamba asali. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Nishati
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa dhati kabisa lakini nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara hii ya Nishati. Waswahili wanasema mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni. Naogopa kusema hapa mimi binafsi au labda kwa sababu ndugu yetu huyu ni Msukuma tabia ya unyenyekevu hii kwake yaani ni ya ajabu kwangu ana unyenyeku uliopitiliza. Wapo waliosema hapa lakini mimi binafsi nasema tu kwamba katika Mawaziri ambao wanaofanya kazi vizuri, kaka yangu Mheshimiwa Kalemani Mungu akubariki sana, umejitoa na unafanya kazi nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nitagusa kidogo kwa habari ya TPDC. Shirika hili la Maendeleo ya Petrolini nchini lilianzishwa mwaka 1969 kwa Amri ya Rais chini ya Sheria ya Mashirika ya Umma (Public Corporation Act). TANESCO wamefanya kazi vizuri sana na wanaendelea kufanya kazi vizuri lakini TPDC nilikuwa najaribu kufanya hesabu hapa huyu mtu aliyezaliwa mwaka 1969 sasa ana miaka 52. Pamoja na mambo mengine inayofanya TPDC hoja yangu ya msingi mpaka leo tunaendelea kufanya tafiti za mafuta miaka 52.

Mheshimiwa Spika, Adolf Hitler mwaka 1945 wakati anakwenda kupigana Vita ya Pili ya Dunia German-Austria pale Linz aliwaita wahandisi akasimama na kusema; nakwenda kupigana vita jangwani nahitaji kupata mashine inayotumia air cooling system akawapa siku saba. Ilikuwa wachague moja, ama awapige bastola ndani ya siku saba wakishindwa kazi hiyo au wagundue mashine ambayo itatutumia air cooling system. Ndani ya siku saba wahandisi wale wa Ujerumani walikuja na majibu ya air cooling system. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, akili ya mwanadamu ilivyo ukiiacha iwe huru inazubaa. Mwanadamu siku zote anataka kusumbuliwa. Ukimtia upepo kidogo anashtuka ndiyo maana hata wakati ule sisi tunasoma darasa la saba ukipigwa fimbo kesho hiyo table unaishika vizuri sana. Namwomba Mheshimiwa Waziri moto ule ule aliotumia TANESCO aupeleke TPDC. Waziri aende TPDC akawaeleze…

T A A R I F A

MHE. CHARLES J. P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, taarifa.

SPIKA: Taarifa.

MHE. CHARLES J.P. MWIJAGE: Mheshimiwa Spika, naomba nimpe Taarifa Mheshimiwa Chifu Kunambi kwamba kwa vigezo na uzoefu wa kutafuta mafuta TPDC haijawezeshwa na haiko kwenye viwango vya kutafuta. Ndiyo maana jana nikawaambia kwamba Uganda 2002 - 2015 walikuwa wamechimba visima 11 ambayo ni confirmatory test ya kutafuta mafuta ilhali Tanzania TPDC wanatuambia wamechimba visima vitatu pale juu, sio namna hiyo.

SPIKA: Mheshimiwa Kunambi, unapokea Taarifa hiyo?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, naipokea Taarifa hiyo lakini bado niendelee kusisitiza tu kwamba Mheshimiwa Waziri sisi Wabunge nadhani kila mmoja hana mashaka na wewe na tunakuombea Mungu aendelee kukubariki na Mheshimiwa Rais aendelee kukuona hivyo hivyo na sisi uendelee kutuhudumia kama Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine namuomba Waziri atusaidie kuhusu gharama za umeme hasa kwa sisi wananchi tunaoishi vijijini. Ni kweli tumekupongeza, unafanya kazi nzuri lakini hii gharama ya Sh.27,000 tafsiri yake kidogo hebu itazame Mheshimiwa Waziri ni pale ambapo kuna nguzo ya umeme na kuleta umeme kwangu au ni pale ambapo unatakiwa kuvuta nguzo nne au sita? Hili kidogo liwekwe sawa.

Mheshimiwa Spika, kwa mwananchi wa kawaida kabisa wa kijijini ukimwambia alipie hizo nguzo sita mpaka kwenye nyumba yake ni vigumu sana. Jana mimi nilipata meseji tatu za wananchi wangu wanaomba niwachangie laki moja moja nao walau wapate umeme. Kama Mbunge sijui utachangia wangapi wananchi zaidi ya 100,000.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili nimwombe Mheshimiwa Waziri atusaidie ufafanuzi anapokuja kuhitimisha hotuba yake jioni ya leo atueleze kuhusiana na suala hili. Watanzania hasa wananchi wa Jimbo la Mlimba wangependa kufahamu gharama hii ya Sh.27,000 inazungumzwa vipi? Ni kuvuta umeme kutoka kwenye nguzo au kuongeza nguzo? Mimi nyumba yangu inahitaji nguzo sita, saba au nane bei hiyo inahusika pia? Kama hoja itakuwa tofauti na hiyo Mheshimiwa Waziri mtusaidie namna gani mnakwenda kama Wizara sasa kufikiri na kutafakari juu ya kupunguza gharama hizi ili kumpunguzia mzigo Mtanzania huyu hasa wa kipato cha chini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri nimemshukuru kwa dhati kabisa na mimi kwangu bahati nzuri tuna mradi ule wa umeme pale Kihansi na tulikuwa tunashuhudia tu umeme unapita unakwenda Dar es Salaam na maeneo mengine leo hii Mheshimiwa Waziri amekwenda kukamilisha pale Mlimba vijiji 11 vilivyobaki, nakushukuru na nakupongeza sana. Hoja inayobaki kwa wananchi wa Jimbo la Mlimba pamoja na kwamba tunakwenda kukamilisha vijiji hivi 11 je, umeme huu utafika kwenye maeneo muhimu kama vile shule, vituo vya afya na zahanati? Haya ni maeneo muhimu sana kwa sababu utaona umeme unapita kwenye njia tu lakini taasisi muhimu kama hizi hazina umeme.

Mheshimiwa Spika, baada ya kusema haya, naomba niunge mkono hoja na Mungu aibariki Wizara hii muhimu. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022 – Wizara ya Maliasili na Utalii
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa dhati kabisa kwa kuwa miongoni mwa wachangiaji. Nitajikita kwenye utalii wa ndani, sote tunafahamu kwamba sekta hii ya utalii ni sekta muhimu na mchango wake kwa Taifa takribani kwenye GDP inachukua asilimia 21. Mimi nieleze tu utaona hapa katika asilimia 21, asilimia karibu 17 ni fedha zinazotokana na watalii kutoka nje ya nchi. Sasa utaona kwa kiwango gani utalii wa ndani haufanyi vizuri.

Mheshimiwa Naibu Spika, nishauri tu, Wizara ya Maliasili na Utalii ijikite kwenye manmade tourism. Manmade tourism itatusaidia, kwa mfano, ukienda kule Dubai una-drive kilometa 100 kutoka city center, kuna eneo unakwenda linaitwa Camel Ride, unafika pale unapanda ngamia tu, unaendesha ngamia, ukitoka unapanda kwenye V8 unaruka ruka. Yaani jambo lenyewe ni la kawaida kabisa lakini watu wanakwenda na wanapata fedha kule Dubai. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niseme tu Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana hii atusaidie. Aongeze thamani ya maeneo yetu ya utalii, kwa kuwekeza kwenye utalii ambao tunauzungumzia manmade tourism.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine watu wengi wamezungumzia migogoro baina ya wananchi na wahifadhi. Naomba niseme hili ni janga la Taifa, hili tulipofikia sasa ni janga la Taifa. Kuna Watanzania wanaishi kwenye nchi hii kama wageni, hasa wanaoishi maeneo ya mipaka ya hifadhi, hawajui kesho yao. Sasa jambo hili lifike mwisho, tutakuwa tunajadili kila siku humu tufike mahali tuseme inatosha. Hatuwezi kuwa tunakaa humu tunajadili kitu hicho hicho wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niishauri Serikali naona hili jambo sio tu la Wizara ya Maliasili na Utalii. Niishauri Serikali, ije na mpango wa pamoja shirikishi. Wananchi washirikishwe lakini twende pamoja, kwa mfano, custodian wa masuala ya ardhi ni Wizara ya Ardhi, Maliasili wao wanakabidhiwa tu kulinda. Leo hii mimi nashangaa kuona Maliasili nao wanakwenda kuweka mipaka, sasa kazi ya Wizara ya Ardhi itakuwa ni kazi gani? Nadhani Wizara ya Ardhi iachiwe jukumu lake, libaki pale pale na kuna baadhi ya maeneo hakuna migogoro, Wizara ya Ardhi imeshafikia imefanya hadi mpango wa matumizi bora ya ardhi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mfano pale kwangu Mlimba Kijiji cha Ijia kimeshasajiliwa kwa mujibu wa sheria na tayari kina mpango wa matumizi bora ya ardhi, lakini mpaka leo wananchi wale wanaishi kama ugenini. Hivi punde wiki iliyopita walikuja hapa wananchi tisa wamelala pale stendi, asubuhi napewa taarifa. Eneo hili halina mashaka, kijiji kimesajiliwa kwa mujibu wa sheria na wananchi wale wangepaswa kuishi bila bugudha. Niombe na niwapongeze pia Waziri wa Ardhi kwa kweli kuna baadhi ya maeneo tayari mipango ya matumizi bora ya ardhi yamekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tushirikiane kazi ya Wizara ya Maliasili na Utalii ni kuomba ramani kwa Wizara ya Ardhi, waende wakazingatie hizo ramani. Yaani hilo jukumu sio la Wizara ya Maliasili na Utalii, Wizara inajipa mzigo ambao isingefaa ijipe, eneo hilo nadhani tulitazame.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa niende katika eneo lingine ambalo pia hapa nimshukuru kwa dhati kabisa Mheshimiwa Waziri. Ametusaidia wananchi wa Jimbo la Mlimba kutoa vibali vya kuvuna mpunga wetu, ahsante sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto inayokuja kwa wananchi wale, naomba, tufanikiwe kwenye eneo hili Mheshimiwa Waziri anapokuja kuhitimisha basi atoe tamko. Wananchi wangu wamekuwa waoga sasa, Meneja wa TAWA anasema njoo uombe vibali, wananchi wanasema wanatuorodhesha ili watukamate tena. Kwa hiyo, hawawezi tena kuvuna. (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba shemeji anapokwenda kuhitimisha bajeti yake atoe tamko kwamba, suala la kuhakikisha wananchi wa Mlimba...

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Kunambi Taarifa Rasmi za Bunge hazitajua nani ni shemeji yako humu ndani.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii ni shemeji yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, niseme tu kwamba, Waziri aje atoe tamko hapa ili awatoe hofu wananchi wa pale Ijia kwamba, Wizara imeruhusu wavune kwa wakati, wakimaliza kuvuna maeneo yale ni vyema sasa yakaendelea na shughuli ambazo zimekusudiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine, nizungumzie kuhusu hawa vyura walioelezwa, vyura ambao wanazaa na kunyonyesha, wapo pale Kihansi Udagali. Sasa niombe tu ndugu zangu Mheshimiwa Waziri atusaidie, kuna watu hawa academic tourism, wakija pale na wenzetu wa TANESCO wamefanya kazi nzuri sana wameweka hadi rest house pale. Kwa hiyo, mtalii akija pale analala vizuri, waje waone academic tourism, waje Mlimba pale Kihansi kuna vyura wanaonyonyesha na wanazaa. Duniani kote hawapatikana wanapatikana pale tu Kihansi.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine ambalo nataka niliseme, kuna hoja hapa ya msingi, nihitimishe kwenye hoja hii ya eneo hili la utalii wa ndani. Tukijiuliza hapa maswali Wabunge wote humu ndani ni wangapi wameshafanya utalii wa ndani hapa? Jibu utakalopata ni wachache kati yetu. Kwa hiyo, nitoe rai kwa Wabunge, tuwe sehemu ya utalii wa ndani, twende tukahamasishe kama mabalozi wa utalii wa ndani ili nchi yetu ipate fedha za ndani.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii na Mungu atubariki sote. (Makofi)
Azimio la Bunge la kuridhia Mkataba wa Uanzishwaji wa Eneo Huru la Biashara la Afrika
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Kimsingi mimi nianze kwa kuunga hoja mkono. Naunga mkono hoja ili nisije nikasahau huko mbeleni. Nianze mchango wangu kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania sasa tunapaswa kubadilika. Tuanze sisi viongozi na Watanzania wote kwa ujumla, tunabadilikaje? Ninavyozungumzia kubadilika namaanisha kwamba tunapaswa kufikiri kimkakati, yaani kila mmoja wetu afikiri kimkakati. Kufikiri kimkakati kutatusaidia kwa sababu kwanza tunakaribisha ushindani na kwenye ushindani maana yake anayeweza kuwa na uwezo katika kushinda atashinda tu, na sisi kwa bahati mbaya sasa, kwasababu hii ni fursa kwetu inaweza ikawa bahati mbaya kwetu sisi tukawa walaji na si wauzaji. Sasa lazima tufikiri kimkakati wote kwa pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe Wizara ya Viwanda na Biashara, Wizara ya Uwekezaji pamoja na Wizara yetu ya Mambo ya Nje. Nianze na Wizara ya Mambo ya Nje. Tuna Balozi mbalimbali kwenye nchi mbalimbali hapa Afrika, Balozi zetu sasa nazo zifikiri kimkakati. Tunao Mabalozi, lakini pia tuna maafisa ambao wapo Ubalozini. Je? tunaowapeleka kule; nimuombe pia Waziri wa Mambo ya Nje, tutazame wale maafisa wetu waliopo huko nje wapo kimkakati? Au tunawapeleka tu kwa sababu waende kutoa huduma kwenye balozi hizo. Nadhani nao tungepaswa kuwapeleka watu ambao wanakwenda kuwa Mabalozi na maafisa ambao wapo kimkakati. Lakini pia na Balozi zetu pia zitumike kimkakati ili kuboresha biashara huko nje ya nchi ambako Balozi zetu zipo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, niende eneo lingine. Nimezungumzia Wizara ya Viwanda na Biashara. Wizara ya Viwanda na Biashara sasa tubadilike na sisi tuwe walezi wa wafanyabiashara wa ndani ya nchi yetu. Kwa mfano; tunaona mtu kama Bakhresa, Azam ukienda takriban nchi zote za SADC anafanya biashara huko, tunaona mfano mzuri. Vilevile tunaona benki ya CRDB leo wapo Burundi.

Mheshimiwa Naibu Spika, watu hawa wanapaswa kulelewa, na wakilelewa hawa wachache wengine watavutiwa na wakivutiwa wengine maana yake pia itaongeza wigo mpana kwa wale wawekezaji nje ya nchi hizi ndani ya Bara letu la Afrika. Kwa hiyo Wizara ya Viwanda na Biashara sasa mnaweza kuwa walezi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano mzuri ni wenzetu China. Kampuni zote za ujenzi zinazokuja kujenga hapa Tanzania kutoka China zinakuwa funded na nchi zao, na China. Zenyewe zinapambana kutafuta tender zikipata tender zinakwenda kwao wanapewa fedha kwa ajili ya kuendelea na miradi ya ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, na sisi yamkini tukashindwa kuwapa fedha hawa wafanyabiashara ndani ya nchi yetu, lakini tuwa-guarantee tu, tunaweza kuwapa dhamana tu, kwamba Serikali ikawa dhamana ya Watanzania wanaokwenda kufanya biashara ndani ya Bara letu la Afrika. Hii itasaidia kwenda kwenye ushindani ambao na sisi utatupa manufaa makubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini eneo lingine nizungumzie suala zima la taasisi za kifedha. Ukiitazama Kenya wana benki kadhaa hapa nchini ikiwemo KCB. Tujiulize Tanzania tuna benki gani kule Kenya? Sasa haya ni maswali ambayo kimsingi yanapaswa kutufikirisha ili na sisi tujipange kimkakati. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia haitoshi, eneo lingine ni kuhusu suala zima la Sera na Sheria zetu, je, sera zetu na sheria zipo katika mtazamo ambao unaweza kutusaidia kama nchi kunufaika na mkataba huu?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo haya ni mambo ambayo nadhani kimsingi tunakwenda kwenye ushindani ambao kimsingi lazima tujiandae. Kwa mfano; tunaweza kuanza na jambo la tunatazama tu kwenye comparative advantage. Kwamba sisi kama Watanzania ni eneo gani tumekuwa mabingwa kwenye uzalishaji na tukatumia eneo hilo kutusaidia ku-compete na wenzetu, mathalani kwenye mazao ya kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, imezungumzwa hapa, na leo tumepata changamoto hapa, ni jambo ambalo wengine watatushangaa. Tukiwa tunajadili kununua mahindi leo hii, yaani dunia inatushangaa, dunia ingetutazama sisi tukiwa tunajadili kuuza unga, kwamba tayari tumeshafanya processing na si mahindi. Sasa tukiona tunafikiri kujadili mahindi tutoke kujadili mahindi tujadili bidhaa ambayo inakwenda kuuzwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, huko Kenya tunakopeleka mahindi tunapata hasara kubwa sisi, hilo lazima mjue. Tunapata hasara kubwa kwa sababu unauza mahindi, kuna pumba na yana vitu vingi ambavyo tunavipeleka Kenya. Kwa hiyo tusiendelee kuuza raw materials tupeleke bidhaa ambazo tayari zimeandaliwa nchini. Na hili haliwezi kufanywa na Serikali, Serikali ibaki kuwa regulator na sekta binafsi sasa iende kwenye ku-capture production. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninayasema haya lengo langu likiwa ni kuona kwamba kama nchi tunakwenda kunufaika na mkataba huu wa eneo huru la biashara ndani ya Bara letu la Afrika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo katika haya narudia kusema kwamba inawezekana, inawezekana tukifikiri kimkakati, na kufikiri kimkakati kutatuwezesha sisi kwenda kuwa washindani kwenye eneo huru la biashara ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. naomba kuunga mkono hoja. (Makofi)
Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021 na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2021
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi nijielekeze moja kwa moja kwenye sekta ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi sekta ya barabara nchini imekuwa na changamoto nyingi sana na hii ni kwa sababu ya kukosa vipaumbele, yaani hatufikiri kimkakati. Nitoe mfano hapa upande wa REA. REA wameanza kusambaza umeme kwenye vijiji vyote na wanahitimisha na sasa wanakwenda kwenye vitongoji. Halikadhalika kwenye barabara tungeiga mfano huu, kwamba leo hii bado nchini kwetu kuna baadhi ya mikoa haijaungana, lakini bado tunakwenda kujenga barabara za wilaya, mimi nadhani hapa tuna-misuse resources. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukilinganisha upatikanaji wa rasilimali fedha na mahitaji makubwa ya barabara nchini hayafanani. Kupanga ni kuchagua. Wachumi wanasema opportunity cost, una-foregone for the best alternative. Sasa, niombe na niishauri Serikali ianze kwa kukamilisha kuunganisha mikoa yote nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mathalan Mkoa wa Morogoro. Mkoa huu katika uchumi wa Taifa letu ni mkoa wa tano katika Pato la Taifa lakini bado mkoa huu mpaka leo haujaunganishwa kwa kiwango cha lami na Mikoa ya Lindi, Ruvuma pamoja na Njombe; na ukiangalia mkoa huu uko kimkakati. Kwa hiyo, niombe tu, kwamba Wizara ya Ujenzi; na niseme kwa dhati kabisa; jamaniee! Katika eneo hili tusi-politicize, tusifanye maamuzi ya kisiasa katika ujenzi wa barabara zetu nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano kuna madhara makubwa sana na hasa ya kiuchumi. Barabara ya mkoa na mkoa wanufaika ni wengi ukilinganisha barabara za wilaya na wilaya. Vile vile kiuchumi barabara ya mkoa na mkoa na wilaya na wilaya ni tofauti kabisa, lakini madhara yake makubwa katika ugawaji wa rasilimali za nchi kunakuwa na uneven distribution of national income, kabisa. Kwa sababu leo hii wilaya na wilaya wana barabara ya lami, ukija Morogoro na Njombe hawana lami, kwa hiyo kuna Wilaya ngapi hazina lami kwa Mkoa wa Morogoro? Ni nyingi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naiomba Serikali, kwa kuwa tunakwenda kwenye kipindi hiki cha bajeti, tuje na mpango wa kukamilisha lami kwenye mikoa yote kwanza ili twende kwenye wilaya. Hii itawatendea haki Watanzania. Mfano mzuri ni wa barabara ya Morogoro – Njombe – Boarder. Barabara hii inaunganisha mikoa za nyanda za juu kusini. Nikitaja mikoa hiyo, ni mingi kweli, mpaka Rukwa mpaka Ruvuma barabara hii kwa sababu inapitia hapa Njombe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, itoshe tu kusema, naishukuru Serikali imeanza kuchukua hatua, ila hoja yangu ya msingi, tunazungumza kwa Habari ya zile kilometa 50, barabara ya Morogoro - Njombe Boader kutoka Ifakara ipite Mlimba iende Madeke – Lupembe mpaka Kibena Junction, barabara hii mpaka sasa naambiwa iko kwenye mchakato wa manunuzi, na mwaka wa fedha unaisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kweli naomba niseme tu kwa dhati, kipindi cha bajeti, Wizara ya Ujenzi ijiandae kisaikolojia, nitashika shilingi. Sitakubali kuona kama lami inayozungumziwa kilometa 50 kutoka Ifakara - Mlimba haijaanza kujengwa. Nitashika shilingi, na nitakuwa wa kwanza. Haiwezekani tunafanya maamuzi ya kisiasa katika mambo ya msingi ya wananchi. Naomba tuanze kuunganisha mikoa ili sasa twende kwenye wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, kuna mtu mmoja anaitwa GN. Huyu GN ni mtu gani? Najiuliza GN yuko sayari gani? Yuko sayari hii au yuko sayari nyingine GN? Huyu ni mtu gani ambaye amekuwa adimu sana kupatikana? Kosa tunalofanya wame-centralize; leo hii GN inatoka TRA Makao Makuu, kwani kudai centralize kuna kosa gani? Si tuna Meneja wa Mkoa wa TRA! Zitoke GN huko. Leo hii miradi karibu 600 anatoa mtu mmoja kule Makao Makuu TRA, ataweza kazi hiyo!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naishauri Serikali na hasa Wizara ya Fedha iachane na ku-centralize mamlaka inayohusika na GN; iji-centralize katika level za mikoa, wanaweza kufanya kazi hiyo ili miradi yetu iendelee haraka. Vile vile procurement process zinakwama sana kwa sababu ya GN, mkandarasi haanzi kazi kwa sababu ya GN. Huyu GN ni mtu gani? Anapatikana sayari ya hii dunia au yuko sayari ya Mars?

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Naomba kuwasilisha. (Makofi)
Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo kwa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Nijielekeze kwenye umuhimu wa kukuza Pato la Taifa letu. Kwa mujibu wa takwimu za Sensa ya Watu wa Makazi ya mwaka 2022 inatanabaisha kwamba idadi ya watu nchini ni takribani milioni 61.7 vilevile inaendelea kusema wastani wa ukuaji wa watu Tanzania kwa mwaka ni wastani wa asilimia 3.2. Nimejielekeza kwenye mpango huu pia unaelekeza kwamba uchumi wetu unakua kwa wastani wa asilimia 5.4. Kwa hiyo, ongezeko la watu lina mahusiano ya moja kwa moja na Pato la Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, actual growth ya Pato la Taifa letu, ukuaji halisi wa uchumi wa Pato la Taifa letu siyo 5.4 ni 2.2 kwa sasa. Unawezaje kupata actual growth kwa maana ya wastani halisi? Unachukua wastani wa Pato la Taifa ambalo ni 5.4 unatoa wastani wa ukuaji wa watu ambao ni 3.2. Kwa hiyo wastani halisi kwa sasa nchini wa ukuaji wa Pato la Taifa ni asilimia 2.2 ambacho kile kimebaki baada ya ku-minus and I stand to be corrected.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa najiribu kueleza tunawezaje kutoka hapa? Tuna kila sababu ya kuongeza bidii kwenye vichochea Pato la Taifa, walau tufike kwenye asilimia nane au kumi. Nilikuwa najaribu kuwaza kwa sauti kama sasa hivi wastani wa ukuaji wa watu ni asilimia 3.2; je miaka hamsini ijayo Tanzania itakua ya aina gani? Tumejipangaje kama Taifa kwa idadi ya vizazi hivyo vijavyo? Bado kuna changamoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nijielekeze kwenye maeneo ambayo tukiwekeza tunaweza kufikia asilimia nane mpaka kumi ya ukuaji wa Pato letu la Taifa. Jambo la kwanza ni utafiti. Utafiti kwenye kilimo, utafiti kwenye viwanda, utafiti kwenye madini, utafiti kwenye masoko na biashara, hali kadhalika na utafiti kwenye mazao ya mifugo ya samaki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa najiuliza pia maswali kuna Chuo kama SUA hivi hatuwezi kubadilisha mfumo wa elimu tukaondokana na tafiti au academic research kwamba ili mtu apate Degree lazima awe amefanya thesis amefanya research fulani lakini ile inaenda kukaa kwenye kabati tu. Sasa hatuwezi kuwekeza kwenye Vyuo Vikuuu tukapata tafiti ambazo ni practical mbona Madaktari wanaweza? Kwa Madaktari wanafanya, Daktari Bingwa wa Moyo anakwenda kufanya tafiti lakini ni practical kwa nini watu wa kilimo wasifanye? Kwamba zao fulani linaweza linaweza likastawi sehemu fulani, ardhi fulani na ikiwezekana na bahati mbaya nilikuwa naona kengele ngoja niende haraka haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeona jitihada za Mheshimiwa Rais, ameenda China tumepata Soko la Parachichi sasa najiuliza maswali tumejiandaaje kukata hiyo market ya parachichi? Kwenye suala la kilimo, tunaona jitihada za sekta ya kilimo lakini tunawekeza nguvu hizi kwenye biashara ya kilimo kimkakati? Kwa mfano, Bonde la Mto Kilombero kuna Bonde la Hifadhi lakini kuna Bonde linalofaa kwa kilimo. Je, tumejifikiriaje kuweka Miradi ya Umwagiliaji? Kwenye Bonde la Mto Kilombero? Tuna mikakati gani ya kuwekeza eneo hilo? Sasa hayo ni mambo ya kuangalia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, nilikuwa nashanga sana leo hii korosho inalimwa Dodoma, Mwanza kila sehemu korosho tu jamani hii korosho inatija gani kwa nchi hii? Tuache Mtwara, walime korosho na sisi watu Mlimba, tuwe na zao maalum la mpunga tuzalishe mchele, lakini navyozungumzia viwanda, nazungumzia viwanda kwa maana siyo vile viwanda vya tunasema viwanda vikubwa nazungunzia agro-base industry ni viwanda vinavyochakata malighafi kuwa bidhaa hiyo ndiyo hoja yangu ya msingi. Tukiwekeza kwenye viwanda maana yake vijana watapata ajira lakini pia tutaongeza Pato la Kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naangalia Urari wa biashara nchini kwenye East Africa tunafanya vizuri na SADC Countries, lakini huko Duniani tuko mbali mno kwenye urari wa biashara ndani ya nchi yetu. Kwa hiyo, tunayo kazi ya kufanya ili tuweze ku-capture hiyo market. Pia kuna urari wa malipo tunasema balance of payment bado tunakwenda kwenye hasi unfavorable balance of payment kama Taifa. Kwa hiyo Mheshimiwa Waziri yupo hapa uchumi, Waziri wa Fedha atusaidie kwenye eneo hili, mipango hii tunayosema sisi basi ichukuliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende mwisho kwenye sekta ya ardhi. Nilikuwa nafuatilia sensa ya watu na makazi idadi ya majengo ni 13,907,951. Idadi kwa maana ya wakati kuna mapitio ya bajeti idadi ya viwanja vilivyopimwa ni Millioni Sita, idadi ya Hati Miliki nchini ni Milioni Mbili. Kwa hiyo kama idadi ya majengo yako Milioni 13 kuna idadi ya watu wenye majengo ambao hawajapimiwa zaidi ya Milioni Saba. Sasa hiyo ni sekta ya sehemu nyingine, pia kuna idadi ukitoa Milioni Mbili watu wenye Hati Miliki maana yake kuna idadi ya Million 11 ya Watanzania hawalipi kodi ya ardhi. Sasa hili eneo ni fursa kwetu nampongeza sana Waziri wa Ardhi anatatua migogoro kwa kutumia hii kliniki, nimeona juzi pale Kibaigwa. Mama anafanya kazi nzuri, kama kutatua migogoro kwa kutumia kliniki na nikuombe Mheshimiwa Waziri, kliniki hii ifanyike na kule Morogoro, isifanyike tu Dodoma. Kliniki endelevu tembezi inasaidia kutatua migogoro.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto tuliyonayo ukiangalia ardhi, nikuombe dakika moja tu nimalizie, samahani ahsante. Tusitazame sekta ya ardhi kama migogoro, migogoro ni matokeo ya kutokufanya vizuri kwa sekta. Kwa hiyo, tukijielekeza kwenye mipango bora ya matumizi ya ardhi hakika Taifa letu litaenda kutatua migogoro yote ya ardhi. Baada ya kusema hayo, ahsante sana na Mungu akubariki sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kuungana na Wabunge wenzangu kumpongeza Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayofanya kuendelea kutuletea maendeleo Watanzania. Lakini kubwa zaidi nimpongeze kwa jambo hili kubwa la Royal Tour kule Marekani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baadhi ya nchi duniani zilikuwa zikiamini Mlima Kilimanjaro upo Kenya, lakini kupitia hii Royal Tour anayofanya Mheshimiwa Rais leo hii dunia inatambua kwamba Mlima Kilimanjaro upo Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, ninaipongeza Wizara. Nianze na Waziri mwenye dhamana na Manaibu wake, Katibu Mkuu, Watendaji na Watumishi wote wa TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi wa Jimbo la Mlimba wameniagiza niwasilishe hoja ya maombi yao ya kuifanya Halmashauri ya Wilaya ya Mlimba kuwa Wilaya kamili. Kwa sababu mwananchi wa Mlimba inamgharimu kutembea umbali wa takribani kilometa 80 kufuata huduma kwenye Ofisi ya Mkuu wa Wilaya. Kwa hiyo, wameniagiza hilo nami nawasilisha hapa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ni kuhusu Kituo cha Afya cha Kata ya Chita. Wananchi wa Mlimba tumeanzisha ujenzi wa Kituo cha Afya cha Kata ya Chita. Katika kituo kile tumeshakamilisha ujenzi wa Jengo la Wagonjwa wa Nje (OPD), maombi yetu ni Wizara kutusaidia kukamilisha ujenzi wa majengo yaliyobaki.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo awali, Mheshimiwa Waziri Ummy akiwa TAMISEMI alitoa ahadi za vituo vya afya kwenye Halmashauri zetu. Na sisi tulipendekeza vituo vya afya viwili, Kata ya Idete na Kata ya Utengule, na hili nakumbusha tu nalo kimsingi kwenye bajeti hii ni muhimu likazingatiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niendelee kwenye suala ambalo limezungumzwa humu ndani, suala la kupanda kwa bei za bidhaa. Limeelezwa humu ndani, nimefuatilia mijadala yote ndani na nje ya Bunge letu lakini pia na majibu ya Serikali. Naomba niseme tu kwa dhati kabisa, haya maswali ya Watanzania ni magumu na majibu yao yanapaswa kuwa yanakwenda kutatua kero zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nimefanya research ndogo tu, unga wa mahindi pale soko la Majengo, kilo 25 hapo awali zilikuwa zinauzwa shilingi 18,000, sasa hivi ni 28,000. Imezidi takribani 10,000. Labda nishauri mambo ya kufanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, Serikali ingetoa ruzuku kwa bidhaa muhimu, hasa za chakula. Jambo la pili, Serikali ingeangalia namna ya kupunguza kodi hasa kwa bidhaa muhimu na kupeleka kodi kwenye bidhaa ambazo siyo za muhimu kwa mfano bidhaa za vileo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kufanya tathmini, bei hizi zina uhalisia? Wasije wakawa wafanyabiashara wengine wana-take advantage kwenye suala la UVIKO na vita ya Ukraine wakapandisha bei maksudi tu. Kwa hiyo, niiombe Wizara ifanye tathmini kutumia Wakuu wa Mikoa na wakuu wa Wilaya ili kuona kama bei hizi zinaendana na uhalisia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni kuhusu suala la machinga. Machinga ni wachuuzi, ni wafanyabiashara wadogowadogo wachuuzi; machinga hafuatwi, machinga anafuata mteja. Nimeona hapa, ukurasa wa 45 kuna Bilioni Tano za UVIKO zimetumika kwenye kujengea maeneo ya machinga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, machinga hawajengewi masoko, tunakosea. Machinga ni mfanyabiashara mchuuzi, ni biashara ambayo ni informal, siyo formal. Sasa ukisema ujenge majengo, mfano Machinga Complex pale Dar es Salaam, nani anakaa pale? Hapa Dodoma mmejaribu tena kujenga, mtakuja kuniambia. Hatuwezi kupunguza watu watakaokaa barabarani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nishauri machinga watengenezewe maeneo rafiki palepale walipo kwa kuboresha. Ukienda Guangzhou, China tutaona wenzetu wanafanyaje. Ukienda pale Dubai ukitoka tu hotelini unakutana na machinga. Duniani kote, miji yote machinga wapo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kupeleka fedha nyingi kujenga masoko ya machinga, machinga yeye ni mchuuzi anatafuta mteja, hafuatwi na mteja. Ukimlazimisha mteja amfuate machinga tunatwanga maji kwenye kinu. Kwa hiyo, niombe kwa dhati kabisa tuachane na mfumo wa kuwajengea masoko machinga, tuwaboreshee mazingira yao rafiki palepale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilijaribu kidogo hapa Dodoma wakati ule kwenye zile barabara. Unatengeneza miundombinu. Kwa mfano kuna watu wa benki, kuna watu wa makampuni ya simu, watengeneze vibanda rafiki ambavyo ni vya muda machinga wakae pale. Lakini pia tuwafuatilie, tuwafanyie tathmini za mara kwa mara. Machinga anatakiwa a-graduate, yaani asiwe machinga miaka yote.

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa.

MWENYEKITI: Mheshimiwa Neema Lugangira, taarifa.

T A A R I F A

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Ninapenda kumpa mzungumzaji taarifa kwamba tulipata fursa ya kwenda kwenye soko hili la machinga hapa Dodoma na tayari machinga 6,000 wameshajiandikisha, wameridhia kwenda pale kwa sababu wamechoka kukaa juani, wamechoka kunyeshewa mvua. Kwa hiyo, huo ni utaratibu mzuri sana wa Serikali ambao imekuja nao. Kama ilivyo kwenye nchi nyingine nasi tutajifunza jinsi ya kuwafuata pale walipo. Ahsante. (Makofi)

MWENYEKITI: Ahsante. Unaipokea taarifa hiyo Mheshimiwa Kunambi?

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi sipokei taarifa. Nataka kusema ninathibisha maneno yangu, mtakuja kuwa mashahidi. Tumefanya Dodoma si ndiyo? Tufuatilie kama tutatoa machinga barabarani. Wataendelea kuwepo barabarani, wataendelea kuwepo maeneo yote, watakuwepo tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ya msingi nikuombe, kwamba machinga hawa waboreshewe mazingira yao maeneo husika. Mheshimiwa Rais amesema wapangwe, sasa sisi tunakwenda kujenga.

Nawaambia, miaka ijayo tutashuhudia machinga hawa wataendelea kuwepo barabarani, maeneo yote ya wananchi. Ahsante. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante. Ningependa kwa dhati kabisa kwanza nimshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoendelea kuifanya katika kuleta maendeleo kwenye Taifa letu. Leo hii niseme kwa dhati kabisa, nimefarijika sana; kwa sababu moja tu, Bunge lililopita nilijenga hoja kwa habari ya jambo la OPRAS. Nilieleza mapungufu ya OPRAS; na nikaainisha mapungufu yote ya OPRAS na leo hii nasema nimefarijika kwa sababu Serikali Serikali hii ni sikivu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali hii ni sikivu kwa maana na nampongeza kwa dhati Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Wizara ya Utumishi na Utawala Bora; amekwenda muda mfupi tu mama yangu huyu, muda mfupi tu, lakini tunaona Wizara inakuja na mabadiliko chanya kwa Taifa hili. Sasa kwa sababu hiyo, nampongeza sana Mheshimiwa Waziri, nampongeza pia Naibu Waziri, lakini nampongeza na Katibu Mkuu Dkt. Ndumbaro, Mwalimu wangu kwa kweli kazi kubwa inafanywa na ni nzuri kwenye Wizara hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze kwenye mchango wangu. Katika hoja yangu niliyoieleza hapo kuhusu OPRAS, wizara au Serikali imekuja sasa na mpango bora kabisa katika upimaji wa utendaji kazi wa Taasisi za Umma ambao naamini unakwenda kuweka tija kwa Taifa letu. Kwanza wamekuja na Mfumo wa PEPMIS (Public Employees Performance Management Information System, mfumo huu ni mfumo ambao unakwenda kuwa mbadala wa OPRAS kwa maana ya kila mtumishi mmoja mmoja anakwenda kupimwa sasa, lakini haitoshi siyo tena kujaza makaratasi, sasa hivi ni mtandao. Kwa hiyo, tunaona watumishi wanakwenda kutendewa haki lakini watawajibika pia.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine wamekuja na mfumo mwingine wa PIPMIS (Public Institutions Performance Management Information System). Mfumo huu, ni mfumo ambao unakwenda kuweka makubaliano baina ya Serikali na Taasisi zake. Jambo hili ni jema ndiyo maana nimesema nimefarijika sana siku ya leo. Sasa katika hili, nimeona nitoe maoni angalau mawili, ni jambo jema lakini nami niboreshe kidogo kwenye maeneo mawili.

Mheshimiwa Naibu Spika, mifumo hii yote miwili imetajwa kwa Kada ya Viongozi wa Kisera. Sasa Viongozi wa Kisera hawa ni kuanzia level ya Wizara, Wakuu wa Mikoa, Wakuu wa Wilaya na kadhalika. Sasa nashauri jambo moja, nashauri kwenye maboresho hayo hayo tuje na KPI, tuongeze KPI. KPI kwa maana ya Key Performance Indicators. Key Performance Indicators ni viashiria muhimu vya utendaji kazi; sasa hivi vitatusaidia hawa Wakuu wa Taasisi kwa mfano; Waziri lazima awe na Key Performance Indicators, kwa sababu tuna Mpango Mkakati wa Miaka Mitano na tuna Mpango Kazi wa Mwaka Mmoja. Tukimpa Waziri kwa mfano, Waziri wa TAMISEMI, akapewa Key Performance Indicators za Mpango Kazi wa Mwaka mmoja alionao, kupitia Mpango Mkakati wa Miaka Mitano, anaweza kupimwa vizuri na Mheshimiwa Rais kuliko kuangalia sasa Vyombo vya Habari kama anakwenda ziara na nini, hii itasaidia sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, halikadhalika kwenye maeneo haya wasimamizi wa Taasisi kwa maana ya viongozi wa kada za utendaji nao wapewe key performance Indicators. Wakurugenzi wa Halmashauri Key Performance Indicators, twende kwenye level ya ma-CEO wa Makampuni au Mashirika ya Umma key performance Indicators; ndani ya mwaka mmoja atatuletea mpango kazi wake na tutampima kupitia mpango kazi aliotulewa na mwisho wa mwaka atueleze kama ame-perform kwa kiwango gani, kama kuna mapungufu aeleze. Mamlaka ya Nidhamu itakuwa sasa na uwezo wa kutathmini kwamba huyu amefeli kwa sababu hatukum-finance au kwa sababu kitendea kazi au rasilimali fedha, amefeli kwa sababu ya uwezo wake. Mwisho wa siku watu wa-vacate ofisi wenyewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa dhati kabisa hii inakwenda kumsaidia Mheshimiwa Rais na nasema kwa dhati. Mheshimiwa Rais sasa hata kuwa na kazi ya kutafuta nani anafanya vizuri na hafanyi vizuri. Nampongeza tena Mheshimiwa Waziri, Mama yangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo, nimesikia kidogo kwamba baadaye tutakwenda biometric, nadhani tusiishie tu hapo. Nilipokuwa hapa Dodoma Mkurugenzi wa Jiji nilianzisha mfumo mmoja, nilifunga camera ofisi zangu zote, kwa hiyo ilikuwa nikikaa ofisini naangalia Idara ya Ardhi nikiwa ofisini, nikiwa kwenye mkutano, nikiwa kwenye kikao chochote namwona mtumishi kwenye ofisi kama anamhudumia mwananchi au anafanya mambo mengine ambayo siyo kwa shughuli zake za kila siku. Kwa hiyo, nilikuwa na uwezo wa ku-detect kila mtumishi, popote nitakapokwenda, nikiwa nakunywa chai naangalia simu yangu, ofisi yangu ipo hapa. Ndiyo siri ya mafanikio hapa Dodoma! (Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nisipoteze sana muda, leo hii nimefarijika sana, naunga mkono hoja na Mungu awabariki watu wa Wizara. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2023/2024 – Wizara ya Kilimo
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Nami nishiriki kutoa mchango wangu, ushauri wangu, kwenye sekta hii muhimu kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Spika, Taifa letu limepita katika kipindi tofauti na katika kila kipindi tulikuwa tunashuhudia kauli mbiu mbalimbali kuhusiana na hii sekta ya kilimo. Wakati wa Hayati Baba wa Taifa tulianza na kilimo cha kufa na kupona, ikapita tukaja na Kilimo uti wa Mgongo, ikapita, tukaja na Kilimo Kwanza ikapita. Sasa tumemaliza maneno yote ya kiswahi tumekuja na maneno ya kiingereza, bado kilimo kipo pale pale ni changamoto kwa Taifa letu, tunasema (BBT) Build a Better Tomorrow (Jenga Kesho Iliyobora). (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mwandishi mmoja wa kiingereza anaitwa Shakespeare aliwahi zungumza kauli hizi mbili; ya kwanza alisema if wishes were horses, baggers would ride them (Kama matamanio yangekuwa Ngami hata omba omba wangeweza kuendesha. Lakini akaaza kuchanganya msemo mwingine tena akisema wishes are weak salad to dine with (matamanio ni sawa na kachumbali iliyochacha haifai kwa kitoweo). (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, tukiendelea kuwa na matamanio kama Taifa kwenye sekta ya kilimo na bila kuwa na jitihada, bila kuwa na utayari, bila kuwa na commitment kwenye sekta ya kilimo, nina wasiwasi hata hii ya BBT (Build a Better Tomorrow). Namwamini sana Kaka yangu Mheshimiwa Bashe na Ndugu yangu Mheshimiwa Naibu Waziri, katika hili wazo ni jema lakini nitashauri hapa tuboreshe kidogo Ili tusiishie tu kuwa na matamanio, matamanio tukumbuke ni sawa na kachumbari iliyochacha haifai kwa kitowewo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nia ni njema na dhamira ya Serikali ni njema kabisa, naomba nishauri kuboresha eneo hili la ajira hasa kwa hawa vijana hii programu ya BBT.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri kaka yangu Mheshimiwa Bashe, naomba unisikie kwa makini eneo hili. Mimi ni mkulima na bahati nzuri na kifahamu kilimo hasa cha zao la mpunga, nililipa ada ya elimu ya sekondari kwa kuuza mchele na mpunga. Nitaeleza kidogo hapo am not speaking from without, am speaking from within. Sizunguzmi habari ambayo siifahamu, nazungumza habari ambayo ninaifahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunawachukua vijana na ninaomba nishauri kufikiri kimakakati kwenye eneo la BBT. Kijana yeyote ni desperate anataka pesa ya chap chap, kijana yeyote anataka maganikio ya haraka. Ukichukua kundi la vijana ukawapeleka mahala tukaandaa mashamba ya block farming, zao ambalo litachukua miaka minne, kijana anakimbia, habaki ataondoka. Kwa sababu matamanio yake apate fedha ya chap chap.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu kwenye eneo hili, twende kwenye maeneo husika ambayo vijana wanajishughulisha na kilimo. Usichukue watu wapya, usichukue watu wa Dar es salaam, usichukue watu wa mjini uwapeleke wakalime, kilimo ni tiresome work sio kazi ya mzaha mzaha ni kazi ya kujituma kweli kweli. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, twende Mororgoro kule Mlimba tukatazame vijana wanajishughulisha na kilimo pale tukawawezeshe wale. Wale wakiwezeshwa, kijana mkulima wa Mlimba anaelima mpunga akalima vizuri, akanunua V8, akajenga nyumba bora anaendesha, vijana wengine watajua kilimo kinalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, lakini hawa watawachukua Dar es Salaam, wamenyoa punk, tunawaweka mahala wakalime kilimo ni tiresome work, sio mchezo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niombe kwanza kufikiri kimkakati jambo moja, aina ya mazao tutakayokwenda kulima yawe ya muda mfupi. Nimeona pale Dodoma ili zabibu ivunwe sio chini ya miaka minne. Nani atakaa miaka minne asubiri hii zabibu? Nina wasi wasi na matokeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, zabibu yenyewe haina soko hapa Dodoma, wananchi mazao yanaoza. Twende tukaimarishe mazao ya muda mfupi. Mahindi, mpunga, kijana ndani ya muda wa miezi minne, au sita ana fedha mfukoni. Mje Mlimba pale mfanye kilimo, muende na maeneo mengine. Mazao ya muda mfupi haya ndio yatakayowasaidia vijana wengi kuvutiwa na kilimo kwa sababu watapata pesa ya chap chap. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine tunazungumzia kilimo cha biashara, ili kilimo biashara kiweze kufanikiwa: -

Mheshimiwa Spika, moja; lazima uwe na ardhi inayofaa kwa kilimo. Sasa na hii ningependa kusikia unapokwenda kuhitimisha, namna gani wizara ya Kilimo inashirikiana na sekta ya ardhi katika kuhakikisha mwananchi wa kitanzania anakopesheka?

Mheshimiwa Spika, leo hii mkulima wa Mlimba ana eneo la heka 50 hakopesheki benki hana title, hawezi kuwa na kilimo biashara. Namshukuru sana Mheshimiwa Rais, kwa
kuwaasa benki zote washushe riba. Ninashukuru benki wameitikia sasa hivi benki mikopo ni single digit asilimia 9. Pia nimekopa juzi CRDB nimekopa wa-vester mikopo mizuri lakini sasa nani anakopesheka? Nimekopesheka kwa sababu nilikuwa nina collateral nina hati. Sasa mkulima wa kawaida asilimia zaidi ya 70 ya wakulima hawana hati miliki. Sasa kilimo biashara itakuwa nikauli ile ile isiyotekelezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, namna gani tunaunganisha sekta ya kilimo na viwanda na Biashara? Hii lazima unapokuja kwenye winding up nipate majibu, unieleze namna gani viwanda na biashara inashirikiana na kilimo katika kuanzisha agro based industries. Hilo nalo ni jambo lingine kwenye suala la zima la masoko. Kwa hiyo, najaribu kueleza haya yote na ni muhimu Mheshimiwa Waziri, ukayaeleza ili tuone kama watanzania kwamba ni kweli tunaona tuko tayari kwenda kuwa na kilimo biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho najua kengele ya pili imegonga, ni ya kwanza naenda ya pili? Ahsante sana.

Mheshimiwa Spika, nilikuwa nazungumzia hoja ya zao la bidhaa ya mchele. Duniani takribani watu bilioni 3.5 wanakula mchele lakini leo hii NRFA hawajajenga hata ghala moja la kuhifadhi mpunga. Mahindi kule Marekani ni chakula cha mifugo. Mahindi yanagharama kubwa kuyahifadhi kuliko mpunga, mpunga hauhitaji dawa yoyote utakaa hata miaka kumi. Adui wa mpunga ni maji tu, mje NFRA na mpango sasa muanzishe maghala ya kuhifadhi mpunga. Hilo ni jambo lingine natoa ushauri kwenye eneo hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni kwenye suala la umwagiliaji. Unajua nasikitika sana kwenda sehemu kame na kuanza kuchimba visima vya maji tutengeneze mabwawa, gharama ni kubwa. Hii nchi Mungu aliibariki jamani yaani hoja yangu tunataka ku–achieve nini? Yaani tunapokuwa na mpango wa jambo fulani tunataka ku–achieve nini? Ushauri wangu kaka yangu Mheshimiwa Bashe, nakuomba nenda maeneo ambayo uwekezaji wa umwagiliaji ni rahisi. (Makofi)

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

SPIKA: Haya ahsante sana, kengele ya pili imekwishagonga.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga hoja mkono. Ahsante sana. (Makofi)
Makadirio na Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na kwa dhati kabisa nianze kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kazi kubwa anayoifanya kwenye Taifa letu kutuletea maendelea Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili nipongeze Wizara kwa maana ya kwanza Waziri lakini na watendaji wote wa Wizara mpaka Wakala wa Barabara kwa maana ya TANROADS, ndugu yangu Mativila, CEO wa TANROADS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze kwenye hoja yangu ya msingi na nianze kueleza kupanga ni kuchagua, rasilimali fedha ni chache lakini tunazitumiaje hizo rasilimali fedha kwenye mambo ya muhimu, wachumi wanasema opportunity cost you foregone for the best alternative. Sasa kuhusu Wakala wa Barabara yaani TANROADS ilianzishwa kwa kusudi kubwa moja, kuunganisha mikoa yote nchini kwa kiwango cha lami. Hiyo ndiyo ilikuwa jambo la msingi kwa Wakala wa Barabara yaani TANROADS.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nizungumze kwa habari ya Mkoa wa Morogoro. Mkoa wa Morogoro, ipo mikoa ambayo haijaunganishwa kwa kiwango cha lami kwa mkoa mmoja, miwili, lakini kwa Morogoro ni mkoa pekee nchini ambao mpaka leo tunazungumza haujaunganishwa na mikoa mitatu. Ukizungumza upande wa Kusini unazungumzia wenzetu wa Lindi, leo hii Mkoa wa Morogoro haujaunganishwa na Lindi kwa kiwango cha lami; ukienda Ruvuma bado Mkoa wa Morogoro haujaunganishwa kwa kiwango cha lami, lakini ukienda Njombe kwa kupitia Ifakara – Mlimba – Madeke - Lupembe pale Kibena Junction kwa maana upande wa Njombe bado Mkoa wa Morogoro na Njombe haujaunganishwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana nimeshukuru hapa, ninashukuru tena kwa mara nyingine, Mheshimiwa Rais ametoa kibali kwa ajili ya kuanza ujenzi walau kwa kiwango cha lami kilometa 50 kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Mkoa wa Njombe. Mnyonge mnyongeni, haki yake mpeni, katika hili Mheshimiwa Rais wanasema ameupiga mwingi, tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo ambalo kimsingi ningependa kulisisitiza hapa ambalo Waziri anisadie wakati anakuja kwenye majumuisho hizi kilometa 50 ambazo tayari tuna kibali za kuanza ujenzi, mwaka ule wa fedha uliyopita zilielezwa kwa habari za kilometa 50 kuanza ujenzi, lakini halikadhalika mwaka huu imejirudia ilikuwa shilingi bilioni saba mwaka huu kuna shilingi bilioni nane.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja yangu kwa Mheshimiwa Waziri Profesa kaka yangu nisaidie wakati unakuja kwenye majumuisho wananchi wa Mlimba wangependa kusikia ni lini mkandarasi atakabidhiwa site kwenye barabara hii. Maana ahadi ya mwaka wa fedha uliopita ilikuwa ni hivyo hivyo haikutekelezwa, mwaka huu pia tumeongezewa kutoka shilingi bilioni saba imekuja shilingi bilioni nane. Sasa hofu yao inaweza ikawa ahadi tu wakati wote. (Makofi)

Kwa hiyo, wanatamani kusikia unapokwenda kwenye majumuisho lini mkandarasi atakabidhiwa site kuanza ujenzi wa barabara hii walau kilometa 50 na zile kilometa 220 ambazo ADB imeonesha nia ya kutusaidia na nimeona imetengwa fedha shilingi bilioni 1.7 kwa ajili ya kufanya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina wa mradi. Kwa hiyo, ninaendelea kusema naishukuru sana Serikali na Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan katika hili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niipongeze Serikali eneo lingine na Mheshimiwa Waziri hili jambo tumechelewa sana. Nimesikia hapa pamoja na barabara zingine kuna barabara inayokwenda kuunganisha Mkoa wa Morogoro na Ruvuma, mfumo sasa wa barabara huu itaenda kujengwa kwa njia ya ubia. Jambo hili tumechelewa sana, wenzetu nchi nyingine huko duniani walishafanya haya mambo. Mimi nadhani sasa umefika wakati tusimame kidete, tusimamie mambo, kwa sababu katika hali ya kawaida nchi yetu ni kubwa, hatuwezi kujenga barabara zetu kwa kiwango cha lami sisi wenyewe kama Serikali. Lakini kwa kutumia ubia ni mfumo mzuri sana ambao ukienda nchi zote duniani wanafanya haya. Sasa naomba jambo hili litekelezeke ili Mkoa wa Morogoro uungane na Mkoa wa Ruvuma kupitia ubia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende eneo la mwisho mchango wangu utaishia hapo; nafahamu lakini kwa sababu Serikali ipo hapa na Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana ya Uratibu wa Shughuli za Bunge yupo, hata kama Waziri wa Fedha hayupo hili ni muhimu nikalisema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto nyingi za miradi yetu ya barabara inachelewa sana pamoja na mambo mengine, upatikanaji wa rasilimali fedham lakini pia uwajibikaji wa watendaji wa Serikali na wakandarasi. Changamoto kubwa nyingine ni changamoto ya kisheria, changamoto ya kisera. Leo hii kuna suala la GN yaani Government Notice, sasa GN inatolewa makao makuu tu pale TRA, sasa nchi hii ina miradi mingapi ya maji, ya barabara yote inatoa Idara moja tu pale TRA. Sasa jambo hili linawezekana kwa nini Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa mujibu lakini mkashauriana na Waziri wa Ujenzi kuona namna bora zaidi ya GN ipatikane kwa wakati, inatuchelewesha sana GN, imekuwa kikwazo kikubwa sana GN. Na kuna wakati niliwahi uliza hapa hii GN niliuliza ni raia anapatikana nchi gani. Lakini ni kitu cha kuamua tu, cha kuamua tu tubadilishe sheria, lakini pia kwenye Sheria ya Kodi Waziri wa Fedha ana mamlaka ya kutengeneza kanuni sasa kama GN sawa wangeweza ku-decentralize kwa maana sasa GN wale Mameneja wa Mikoa wa TRA wakasimiwe majukumu haya ya kutoa GN katika level za mikoa ili fast track miradi. Ni jambo la kuamua tu. (Makofi)

Sasa leo mkandarasi GN, mwezi mmoja amesaini mkataba GN, miezi miwili GN, hapana tunamkwamisha Mheshimiwa Rais. Jambo hili ni la kuamua tu. Nadhani Serikali imesikia katika hili na kwa leo niseme tu kwa dhati sina mengi ya kusema nimehemewa na wananchi wa Mlimba wamefurahi sana.

Mwishoni Mheshimiwa Waziri tukimaliza Bunge wangependa kukusikia ni lini unakwenda pale kuzungumza na mkandarasi aanze kazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya naipongeza sana Wizara hii, Mungu awabariki sana, ahsanteni sana. (Makofi)
Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2022/2023 – Wizara ya Nishati
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Mimi nianze kwanza kwa namna ya pekee kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuona umuhimu wa kupeleka fedha takribani Shilingi Bilioni 100 kwa ajili ya kunusuru suala hili la upandaji wa bei ya bidhaa hii ya mafuta. Nimpongeze Waziri na Wizara yake na Watendaji wote wa Wizara na Taasisi ambazo ziko chini ya Wizara hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nianze kuishauri Serikali kupitia Wizara hii muhimu. Tunachangamoto kubwa hasa kwenye suala la gharama za kuunganishwa na huduma ya umeme kwa mwananchi mmoja mmoja lakini pia na taasisi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashauri leo hii kwa nini Serikali isije na mpango huu kwamba mwananchi anapotaka kuunganishwa na huduma ya umeme, asilipe chochote aunganishiwe gharama halafu aje kutozwa hiyo gharama kwenye bili yake ya kulipia umeme kama huduma zingine. Kwamba unaunganishiwa umeme bure, ukishaunganishiwa umeme unapotaka kuingiza umeme kwa maana ya LUKU, basi unalipa gharama yenu mnakata humo kidogo kidogo, hii niwaambie mkiweza kutekeleza hili litasaidia, kwanza mtaongeza wigo ya wateja wengi wataunganishiwa umeme watu wote wenye mahitaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia upande wa pili mwananchi ataona unafuu kwamba anaunganishiwa umeme bila gharama yoyote. Sasa hivi tunaombwa sijui Shilingi 27,000, sijui Shilingi ngapi inatupa shida tu. Lakini Mheshimiwa Waziri wewe ni Kaka yangu najua wewe ni fresh minded na unafikra nzuri, nikuombe katika hili jambo hili ukilifanya kwa kweli kama Wizara yako inakwenda kupata credit, kubwa zaidi na Serikali inakwenda kuongeza wigo wa mapato kwamba kundi kubwa la wananchi, wataunganishiwa umeme, pia ulipaji utakuwa kwenye gharama zake kwa maana ya bili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine la pili ninashauri kwamba tumeona wengi tunatumia television kuna ving’amuzi mbalimbali, Azam sasa hivi nikiunganisha tu huduma ya Azam moja kwa moja napata huduma na napata huduma ile ya television, leo hii LUKU kwa kutumia hizi LUKU zetu za TANESCO kwanza unanunua umeme halafu unakwenda unaanza kubofya tena kuunganisha umeme, hii teknolojia imepitwa na wakati kwa kweli, jambo hili mimi nadhani halileti afya. Kama kwenye ving’amuzi tunaweza kwa mfano mimi leo hii niko Jimboni, mlinzi ameniambia umeme umekatika na nimefunga nyumba yangu LUKU iko ndani, maana yake nini, ninaweza kuunganisha umeme nikiwa Jimboni Morogoro hapa Dodoma nyumba yangu ikawaka, jambo hili linafanyika na ni jambo la kawaida tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niombe kushauri Serikali ni vyema ikaja na mpango huu hii ndiyo teknolojia ya kisasa na naamini Wizara ikienda kufanya jambo hili itasaidia na sisi wananchi kupata unafuu wa huduma hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niguse eneo lingine la mradi wa REA mimi Jimboni kwangu ninaishukuru Serikali mradi huu unatekelezwa kwenye vijiji 11, lakini changamoto kubwa ambayo tunaipata wananchi wa Mlimba ni Mkandarasi. Kwa mfano, kuna Kijiji cha Lugala na Kaka yangu Mheshimiwa Waziri mpaka leo huyu Mkandarasi hata kuchimba mashimo hajachimba hata nguzo wananchi wa Lugala hawazioni pale Uchindile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa muda bado na mnasema Disemba mradi unakamilika, lakini kama hajaanza kazi hofu yangu anaweza akaomba tena extension. Kwa hiyo, jambo hili mimi niombe kwamba kwa Wizara ni muhimu sasa likachukua hatua kwenye eneo hilo, hali kadhalika Kijiji cha Tanganyika pale Masagati kuna hiyo changamoto. Kama haitoshi nimesikia sikia kama ni kweli au la na kama ni kweli Mheshimiwa Waziri nikuombe unapokwenda kufanya majumuisho, nimesikiasikia mnataka kutuongezea ile Low Voltage (LV) kwenye vijiji vyote ambavyo viko kwenye hii miradi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kuna huo mpango Serikalini kwenye Wizara yako kwamba, mnatuongezea kilomita nyingine katika hili nianze kukupongeza kabla hujasema. Kwa kuwa, imekuwa ni changamoto kubwa sana kule kwenye vijiji vyetu, LV umeme mdogo unakuwa na kilomita moja haufiki maeneo muhimu, lakini kama mnakwenda kutuongezea ushauri wangu mwingine ni muhimu sasa umeme huu uguse kwenye maeneo muhimu ya huduma za jamii. Kwa mfano, vituo vya afya, zahanati na shule zetu, hii itatusaidia wananchi hawa kupata huduma, kwa hiyo kama kuna jambo la namna hiyo Mheshimiwa Waziri kwetu sisi wana Mlimba tunasema ukiweza kutuongezea hiyo kilomita moja, unapokwenda kuhitimisha hapa sisi tutashangilia na kwa kweli utakuwa umeupiga mwingi sana Kaka yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la mwisho ni eneo la suala la utafiti wa mafuta na gesi nchini. Nchi yetu ni tajiri sana isingefaa tuendelee na changamoto za mafuta, isingefaa tuendelee na changamoto za umeme. Mimi nishauri jambo hili inawezekana na niliwahi kusema hapa huko nyuma nchi yetu ina kila kitu, hatuna changamoto ya rasilimali fedha wala rasilimali watu changamoto tulizonazo ni tatu tu kama nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya kwanza ni uzalendo, Mtanzania yeyote mwenye mapenzi mema na nchi yake anaweza kufanya jambo kubwa sana. Pili, ni mindset kwamba it can be done, inawezekana! Watanzania wengi hatuna jambo hili. Jambo la Tatu, ni commitment. Mtu yeyote kwenye Taasisi yoyote akiwa na mambo haya matatu anafanya miujiza. Tumekuwa tukizungumza fedha fedha fedha jambo moja, lakini uzalendo, tukiweka mbele mindset kwa maana ya positive attitude na mwisho commitment inawezekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo niseme tu na nishauri Wizara hii na ninaamini naendelea kusema my brother naamini uwezo wako naujua, nafahamu pia na uwezo wa Naibu Waziri wako, katika hili nadhani mnayo nafasi bado. Mnayo nafasi Watanzania tunayo imani na ninyi kwa kutumia hayo mambo matatu naamini, mnakwenda kufanya miujiza kwenye Wizara hii na sisi wote Watanzania tukafurahia huduma ya Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninakushukuru sana ahsante sana. (Makofi)
Muswada wa Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali (Na 2) wa Mwaka 2021 (Toleo la Kiingereza)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze mchango wangu kwa kutoa pongezi za dhati kabisa kwa Wizara ya Katiba na Sheria lakini pia kwa Wizara ya Ardhi, kuna eneo hapa wamenifurahisha ku-address changamoto moja kwa wananchi na nitaieleza baadaye.

Mheshimiwa Spika, naomba niaze mchango wangu moja moja kwa kujielekeza kwa mchango alioutoa hapo awali dada yangu Mheshimiwa Dkt. Pindi Chana, ningekuwa mimi ile Taarifa nisingeipokea, sio Taarifa sahihi, yeye alikuwa sahihi zaidi kuliko mtoa taarifa.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu alichokisema yeye naomba Regional Advocates Ethics Committee, niseme vizuri there is establishment in each region, the Regional Advocates Ethics Committee, end of quote. Ninamaanisha nini? Yeye alichokuwa anasema hiki kipo hapa kwenye regional level anaomba pia neno ethics litumike kwenye National level.

Mheshimiwa Spika, lakini akasema kwenye schedule of amendment ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali bado ameondoa ethics, amebaki na mtazamo wa kuwa naomba nieleze basii…

SPIKA: Umsikilize Mheshimiwa namlinda, ongea na mimi Mheshimiwa.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, kwenye schedule of amendment ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali ameondoa neno ethics, ethics ameondoa, ameondoa maana yake nini? Hatuna neno ethics kwenye Regional Level au National Level. Ndiyo hivyo, kwa hiyo yeye anasema mchango wake neno hili litumike pande zote mbili. Kwa hiyo, amempa taarifa ya uongo tu. (Makofi)

SPIKA: Tukifika kipengele hicho mtatukumbusha enhee tuone vizuri.

MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Spika, nilikuwa naona taarifa sahihi kwenye eneo hilo, naomba niende kwenye mchango wangu.

Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye mchango wangu kwenye eneo la marekebisho hasa kwenye eneo la Mabaraza ya Ardhi ya Wilaya. Changamoto kubwa zitatukuta kwenye eneo hili huko mtaani kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, la kwanza, lilikuwa ni ucheleweshwaji wa mashauri haya kwenye level za Mabaraza ya Kata. La pili, ambalo nadhani nitoe ushauri kwa Serikali wakati ujao litazamwe hili pia. Changamoto ya pili, ni kutofika eneo la mgogoro kwa wenyeviti wetu wa Mabaraza haya ya Wilaya ya Ardhi. Changamoto ya tatu, ni mawanda ya ushahidi wa mashauri haya ya Ardhi.

Mheshimiwa Spika, katika utaratibu wa kawaida wa kusikiliza mashauri haya kwenye level za Mabaraza ya Kata, yakishasikilizwa sasa hoja yangu ambayo ningependa nipate ufafanuzi, hii sheria ilivyoleta ime-address changamoto moja ya kuharakisha ucheleweshaji kwamba wakichelewa ndani ya siku 30 huna sababu ya kusubiri Baraza la Kata tena nenda wilayani, jambo jema ambalo nalipongeza kwa Wizara na Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Wizara ya Katiba na Sheria.

Mheshimiwa Spika, ninachoomba kwa Serikali wakati ujao na hili wanaweza kulitazama upya, kwamba namna gani liwe takwa la kisheria kwamba Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya atakwe lile takwa la Kisheria kwenda kwenye eneo la mgogoro. Sasa hivi ana hiari ya kwenda au kutokwenda, sasa tatizo na mgogoro wa ardhi changamoto ni eneo la mgogoro. Anaweze akaamua tu akiwa mezani lakini asione upana wa tatizo lenyewe. Kwa hiyo, nadhani Mwanasheria Mkuu wa Serikali pamoja na Wizara ya Katiba na Sheria lakini kwa kushirikiana na Wizara ya Ardhi mlitazame hili katika kipindi kijacho.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni suala la ushahidi, sasa hapa pia nahitaji ufafanuzi Mheshimiwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Imeelezwa tu kwamba ikicheleweshwa ndani ya siku 30 anapaswa kukata rufaa siyo kukata rufaa anakwenda ku-proceed anaanza kama fresh complaints au anakwenda kama rufaa yaani isiposikilizwa anakwenda kuanza upya, lakini je nikisikilizwa na sijaridhika na haki yangu katika ngazi ya Baraza la Kata inakuwaje? Inakwenda kama rufaa au nakwenda kuanza upya na kama inakwenda kama rufaa, hoja yangu ya msingi hapa mawanda ya ushahidi yanafungwa.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kesi ya msingi kama ikishaikilizwa kwa level ya Baraza la Kata, nikikata rufaa kule Mwenyekiti wa Baraza la Ardhi la Wilaya yeye hana nafasi ya kufokea tena ushihidi, kwa hiyo ataendelea tu kwa maamuzi yaliyofanyika kwa watu ambao hawana taaluma ya sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ombi langu kipindi kijacho kama hilo pia litatazamwa kwa upande wa Serikali waje na utaratibu ambao unaeleza kwamba mgogoro ule kwenye level ya kata kuamuliwa, sasa sijui utaratibu gani utumike yaani kule uende mgogoro upya ili ufungue mawanda ya ushahidi kwa wale wataalamu wa sheria ngazi za mabaraza wa pale.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ni eneo hili la Regional Advocates Ethics Committees. Utamaduni wa leo katika mahakama za kawaida za wilaya, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya wamekuwa Wenyeviti wa Kamati za Nidhamu ngazi ya wilaya kwa mahakimu na ngazi ya mikoa kwa Wakuu wa Mikoa kwa mahakimu ndani ya mkoa.

Mheshimiwa Spika, ombi langu katika hili ambalo linahusu mawakili, niiombe Serikali kama itaona inafaa kwa nini Wakuu wa Mikoa hata wawe tu co-opted member inawezekana siyo mwenyekiti, mwenyekiti anaingia kuwa Registrar lakini Mkuu wa Mkoa kwa sababu ana dhamana ya upande wa maeneo hayo ya migogoro ya ardhi awe kama sehemu ya mjumbe yaani co-opted member. Kama siyo co-opted member, siyo mjumbe kamili kwenye eneo hilo lakini Registral aendelee kuwa mwenyekiti ili asije akafanya intervention kwenye maamuzi. Kwa hiyo, ombi langu kwenye ngazi ya mkoa kwa sababu inaishia kwenye level ya mkoa basi, Wakuu wa Mikoa wapate fursa ya kuwa wajumbe kwenye haya Mabaraza yanayohusu Mawakili.

Mheshimiwa Spika, kengele ya pili? Ya kwanza!

Mheshimiwa Spika, eneo la lingine nijielekeze kwenye marekebisho ya Sheria ya Usimamizi wa Mazingira. Nimeona hapa kuna eneo linaelekeza kwamba anaruhusiwa, inasema hivi; naomba ninukuu:-

“Notwithstanding the provision of sub-section one the Director General may in addition to the fine in cause under sub-section one applies to the court pursuant to the section 193 for feature of any instrument article vehicle or other thing if any respect of which the offence has been committed.”

Mheshimiwa Spika, naona hapa kama kuna adhabu mara mbili, sijui, lakini naona kama kuna adhabu mara mbili, kwamba capitally kuna fine pale juu halafu tena juu hapa bado anaweza akachukuliwa mali zake, nadhani hii itazamwe kwenye Serikali. Kwamba tayari umemtoza mtu faini wakamuhukumu kwenye compound offences aka-clear kila kitu lakini bado kuna fursa ya mtu mwingine Director General anapata fursa ya kuomba hatamu zile mali zake tena anyang’anywe. Hii sidhani kama linaweza kuwa na afya kweli kwenye jamii zetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, michango yangu ni hiyo kwa siku ya leo. Lakini ningeomba pia Serikali initolee ufafanuzi kwenye maeneo haya mawili muhimu ili la Wakuu wa Mikoa lakini na hili la hizi compound offences pale ambapo tunaona kuna adhabu mara mbili. Ahsante.
Muswada wa Sheria ya Fedha wa Mwaka 2020 (Toleo la Kiingereza)
MHE. GODWIN E. KUNAMBI: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante. Nijielekeze moja kwa moja, kwenye mchango wangu nianze na Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Sura namba 178. Katika eneo hili kwanza naipongeza Serikali, pia nampongeza Waziri, Mawaziri wote wawili wa Fedha na wa Elimu. Hata hivyo, katika eneo moja tu ingefaa tuishauri Serikali wakati tunakwenda kuipitisha Muswada huu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nianze kwa kunukuu hotuba ya Mheshimiwa Waziri, kwenye ukurasa wa sita anasema hivi, Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Sura ya 178 inasema hivi; Sehemu ya Saba kama ilivyorekebishwa, inapendekeza marekebisho kwenye kifungu cha 7 cha Sheria ya Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Sura ya 178, ili kuweka mashari kwa Bodi ya Mikopo kutoweka ada au tozo yoyote ikiwemo value retention fee kwenye mikopo ya wanafunzi kabla ya kupata idhini ya Waziri mwenye dhamana ya masuala ya Elimu baada ya mashauriano na Waziri mwenye dhamana ya masuala ya fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, utakubaliana nami kwamba, dhamira ya Serikali ni njema sana, lakini hapa kwa lugha ya kisheria, Kiingereza lakini pia ya kisheria, hii inaitwa clawback clause. Tafsiri yake ni nini?

Mheshimiwa Naibu Spika, unapoweka takwa la masharti maana yake unampa mtu haki kwenye mkono mmoja, halafu unamnyang’anya kwa mkono mwengine. Unavyoweka masharti Bodi ipate kibali cha Mawaziri hawa wawili baada ya mashauriano hii ni clawback clause, maana yake unatoa haki kwa mkono wa kushoto na unainyang’anya kwa mkono wa kulia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niombe tu Mheshimiwa Waziri katika hili, nadhani tupate maelezo hapa. Mapendekezo yangu ni kwamba, tunapotoa katazo la namna hii kwa mujibu wa sheria libaki hivyo ili tusitoe haki kwa mkono wa kushoto na kuinyang’anya kwa mkono wa kulia.

Mheshimiwa Naibu Spika, niende eneo lingine la Sheria ya Rufaa za Kodi, Sura ya 408, naomba ninukuu tena, ukurasa wa 13 kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Sehemu ya Ishirini na Tatu inapendekeza marekebisho kwenye kifungu cha 22 katika Sheria ya Rufaa za Kodi, Sura ya 404 ili kuanzisha utaratibu wa kufanya usuluhushi wa migogoro ya kikodi nje ya Mahakama. Hoja yangu hapa utaratibu huu ni upi? Huu utaratibu mwingine ambao sasa tunasema tuutumie kuondokana na jambo la kupeleka kesi Mahakamani, nashauri pia, eneo hili ingefaa tupewe maelezo mengine ya kueleza utaratibu huu husika unakwenda kutumika sasa. Ukisema tunaandaa utaratibu tu, katika hili tunaacha ombwe. Yamkini sasa tunafuta Mahakama na sasa hatuna rufaa kabisa za kikodi, kwa hiyo atueleze tu utaratibu ambao Serikali inatuletea ni upi.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nijielekeze pia kwenye eneo lingine la Sheria ya Kodi za Majengo, Sura ya 289. Naipongeza Serikali, kwanza kwa kupunguza kodi mpaka kufikia Sh.1,000 kwa nyumba za kawaida na kwa nyumba zenye ghorofa kwa maana ya kila ghorofa litatozwa Sh.5,000. Hilo ni jambo jema sana. Hoja yangu ya msingi, ni kweli tunapambana na mapato, changamoto ninayoiona tunapambana na mapato katika vyanzo vilivyopo, yaani hatufungui wigo mpana, hatufikiri tofauti kupata vyanzo vingine vipya.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna maelezo hapa ya kuongeza wigo wa kodi, lakini ukiangalia katika uhalisia huoni kodi zipi zimeongezeka, wigo huu ni wa wapi? Vyanzo vipo, naomba nipendekeze katika jambo hili; kuna wafanyabiashara wa nyumba za kupangisha, hawa wanalipa kodi gani, yaani mpangaji anavyolipa kodi ya mwaka Serikali inapata nini, kwa sababu nayo hay ani mapato yake. Hiki ni chanzo kingine tunakiacha na watu wanakwenda huko wengi, kwenye apartment na nyumba za kupangisha wanalipa kodi gani zaidi ya proper tax. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani pia tuliangalie eneo hili, huku kuna fedha pia, tusiache fedha hizi zipotee, tuishauri Serikali, Mheshimiwa Waziri wa Fedha tuangalie eneo hili hata kama sio leo, basi wakati ujao waone chanzo hiki muhimu, kwenye tax base. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo lingine nishauri pia ni suala zima la Sheria ya Kodi ya Mapato, Sura ya 232. Tumeona hapa, naomba niishauri Serikali, kuna kitu tumekiacha hapa. Kuna tozo hii ambayo nadhani pia wananchi wanaumia sana, tozo ya ongezeko la mtaji yaani capital gain tax. Unapofanya transfer ya jengo au kiwanja unapaswa ulipe asilimia 10 ya kipato ulichokipata. Kwa mfano, mwananchi akiuza nyumba yake kwa bilioni moja anapaswa ailetee Serikali milioni 100, je, nani yupo tayari na mwaminifu wa kiwango hicho? Milioni 100 kuipeleka Serikalini tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, nilikuwa naangalia Kenya, wenzetu wanatoza five percent. Kwa hiyo, niishauri Serikali kama sio leo kwenye Muswada huu na hii spoon food for thought, awamu ijayo watakayokuja, katika eneo hili pia wawapunguzie mzigo Watanzania. Niseme tu kuna multiplier effect hapa, ukipunguza 10 percent ya capital gain tax kwenda kwenye five percent, utahamasisha biashara ya kwenye sekta ya ardhi, majengo na maeneo mengine.

Mheshimiwa Naibu Spika, hii haitoshi, kwa sababu kwa mfano mwananchi ana kiwanja hawezi kukiendeleza, kuna mfanyabiashara anataka kujenga hoteli anakuja kununua na bahati nzuri sasa multiply effect itapatikanaje, atajenga jengo la hoteli tutapata na kodi zingine huko. Kwa hiyo, hata Sekta ya Ardhi kwenye uwekezaji itakua kwa kiwango cha juu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo naomba kuunga mkono hoja. Ahsante sana. (Makofi)